Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi 
Mahmoud Thabit Kombo (Mb) ameongoza ujumbe wa Tanzania katika Kikao cha 
Kwanza cha Mashauriano ya Kidiplomasia kati ya Jamhuri ya Muungano wa 
Tanzania na Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) kilichofanyika Makao Makuu 
ya Wizara ya Mambo ya Nje ya UAE mjini Abu Dhabi tarehe 05 Desemba 2024.
Kupitia
 mazungumzo hayo ya kwanza na ya aina yake, Tanzania na UAE 
zimehakikishiana dhamira zao za kuendelea kushirikiana kwa karibu 
kuboresha uhusiano uliopo ili kuufikisha katika viwango vya juu kwa 
manufaa ya nchi na wananchi wa pande zote mbili.
Aidha, Tanzania 
na UAE  zimeongelea pia umuhimu wa kushirikiana kiuchumi na kuwa na 
ushirikiano wa kina uliojengwa juu ya msingi wa kuaminiana, ambao 
umeyafanya mataifa haya kushirikiana kwa karibu katika kushughulikia 
masuala mbalimbali ya pande mbili na ya kimataifa kwa maslahi ya pamoja
Pamoja
 na mambo mengine kupitia mashauriano hayo Tanzania na UAE 
 zimekubaliana kuendelea kushirikiana katika sekta mbalimbali ikiwemo 
biashara , uwekezaji, Kilimo, Mifugo na Uvuvi hususan kwenye mpango wa 
Tanzania wa Build Better Tomorrow (BBT), Ujenzi na Usafirshaji, Nishati;
 Afya na Uchumi wa Buluu.
Aidha, kwa upande wa Nishati UAE 
imekubali ombi la Tanzania la kuunga mkono Agenda ya Nishati Safi ya 
Kupikia (Clean Cooking Initiative) inayopewa msisitizo na Rais wa 
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na kuungwa
 mkono na Wakuu wa Nchi na Serikali wa Afrika na Dunia kwa ujumla kwa 
kuwa sio tu unamkomboa Mwanamke lakini pia inachangia katika agenda ya 
Dunia ya utunzaji wa mazingira.
Katika kutekeleza makubaliano 
tajwa pande zote mbili zimekubaliana kukamilisha na kusaini mikataba 
mbalimbali ya ushirikiano hususan ya ya kiuchumi kwa maslahi ya wote.
Sambamba
 na hilo, Tanzania na UAE  zimekubaliana kuharakisha utekelezaji wa 
mradi wa Upanuzi na Ukarabati wa Hospitali ya Wete, Pemba ambayo 
inatekelezwa kwa ufadhali wa Mfuko wa Maendeleo ya Abu Dhabi kwa gharama
 ya Dola za Marekani Milioni 10 pamoja na utekelezaji wa Mkataba kati ya
 Mfuko wa Maendeleo wa Khalifa (Khalifa Fund) na Serikali ya Mapinduzi 
ya Zanzibar ya Msaada wa Dola za Marekani Milioni 10 kwa ajili ya Miradi
 ya Wajasiliamali Wadogo na Wakati Zanzibar.
Akizungumza katika 
majadiliano hayo Naibu Waziri wa Mambo ya Nje anayeshughulikia masuala 
ya siasa wa UAE Mhe. Lana Nusseibeh alisema Tanzania ni moja ya wadau 
wakubwa wa UAE barani Afrika na kuongeza kuwa hali hiyo imesababisha 
kusainiwa kwa Mikataba ya Ushirikiano katika Sekta ya Anga na Kutotoza 
Kodi Mara Mbili .
Kupitia mikataba hiyo Mashirika ya Ndege ya 
Emirates, Etihad na FlyDubai pamoja na Air Tanzania yamepata kibali cha 
safari za moja kwa moja kati ya nchi hizi mbili.
Kikao hicho
 cha kwanza cha mashauriano ya kidiplomasia kimekuwa cha mafanikio na 
kimefanyika wakati ambapo Tanzania na UAE zinaadhimisha miaka 50 ya 
uhusiano wa kidiplomasia  na sasa umejikita katika ushirikiano wa 
kiuchumi kwa maslahi ya pande zote mbili.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi 
Mahmoud Thabit Kombo (Mb) akiongoza ujumbe wa Tanzania katika Kikao cha 
Kwanza cha Mashauriano ya Kidiplomasia kati ya Jamhuri ya Muungano wa 
Tanzania na Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) kilichofanyika Makao Makuu 
ya Wizara ya Mambo ya Nje ya UAE mjini Abu Dhabi tarehe 05 Desemba 2024.Ujumbe
 wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE )katika mashauriano hayo uliongozwa 
na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje anayeshughulikia masuala ya siasa wa UAE
 Mhe. Lana Nusseibeh


 




Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...