Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela (kulia) akimkabidhi zawadi Mkurugenzi mteule wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika, Profesa Mohammed Janabi kumtakia utumishi mwema wa majukumu anayoenda kuyaanza hivi punde. Hafla hiyo fupi ilifanyika katika Hospitali ya Taifa Muhimbili sambamba na kuwafungulia Akaunti ya Junior Jumbo Watoto 76 waliozaliwa hospitalini hapo.

 
Mkurugenzi mteule wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika, Profesa Mohammed Janabi (kushoto) akimsikiliza kwa umakini Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela (kulia) alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kumuaga na kumtakia kazi njema katik amajukumu yake mapya anayotaraji akuyaanza hivikaribuni.

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela (kulia) na Balozi wa Akaunti ya Junior Jumbo ya Benki ya CRDB, Paula Masanja (kushoto) wakimkabidhi mmoja wa wanawake (katikati) waliojifungua katika Hospitali ya Taifa Muhimbili zawadi kwa ajili ya mtoto wake kuadhimisha Wiki ya Mtoto wa Afrika.  
 
====  ====  ==== 
 
Dar es Salaam. Tarehe 19 Juni 2025: Katika kusherehekea Siku ya Mtoto wa Afrika inayoadhimishwa Juni 16 kila mwaka, Benki ya CRDB imetembelea wodi ya watoto katika Hospitali ya Taifa Muhimbili na kuwapongeza wazazi kwa kujifungua salama.

Licha ya ziara hiyo iliyofanyika katika wodi ya watoto njiti hospitali hapo, Benki ya CRDB pia imetumia nafasi hiyo kumuaga aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Profesa Mohammed Janabi kwa kushinda kiti cha Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika.

Akizungumza kwenye ziara hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela amesema siku zote wamekuwa wakitoa elimu ya fedha na kuwahamasisha wananchi kutumia huduma za benki tangu wakiwa wadogo ili kujenga msingi imara wa uchumi binafsi siku zijazo.

“Katika wiki hii ya kuadhimisha Siku ya Mtoto wa Afrika tumeona ni vyema kuja kuzungumza na wazazi hapa Muhimbili. Tunasisitiza elimu ya fedha ianze kutolewa tangu kwa watoto wadogo na ili kuliweka suala hili kwa vitendo, watoto wote waliopo hapa tutawafungulia Akaunti ya Junior Jumbo yenye shilingi 10,000 ya kuanzia ili mzazi akitoka hapa akaendeleze utaratibu wa kumtunzia mwanaye fedha zitakazomsaidia siku zijazo,” amesema Nsekela.

Kwa akiba yoyote iliyomo kwenye Akaunti ya Junior Jumbo, Benki ya CRDB hutoa riba ya mpaka asilimia 5 kwa mwaka hivyo kumpa uhakika mzazi au mlezi uhakika wa fedha za uhakika pindi mwanaye atakapoanza shule au atakapokuwa na mahitaji mengine yanayohitaji fedha.

“Akiba inawekwa kidogokidogo ingawa matumizi yake huwa makubwa pale yanapojitokeza. Ni vizuri kujenga utamaduni wa kuhifadhi fedha kidogo ambazo kadri muda unavyoenda zitazidi kuongezeka hivyo kutosha kwa ada na matumizi mengine ya shule au kwa jambo jingine ambalo mzazi atahitaji kulifanya kwa ajili ya mtoto wake,” amesema Nsekela.

Akimuaga Profesa Janabi anayetarajia kuondoa wiki ijayo kwenda kuanza majukumu yake mapya na Shirika la WHO hivi karibuni, Nsekela amemsifu kwa mikakati makini aliyonayo na kumuahidi kwamba Benki ya CRDB ipo tayari kushirikiana naye huko na anakokwenda na itaendeleza uhusiano mwema uliopo na Hospitali ya Taifa Muhimbili hata baada ya yeye kuondoka.

“Nilikusikiliza wakati wa kampeni za kuomba uchaguliwe kuiongoa WHO. Ulikuwa na mikakati 10 lakini mimi nimevutiwa na tatu ambazo ni utafiti na ubunifu, ubia pamoja na ufadhili wa huduma za afya kwa vyanzo vya ndani. Naamini vipaumbele hivi sio tu vitazifaa nchi zote 47 utakazokuwa unazihudumia bali vinato anafasi kwetu sekta binafsi kushiriki zaidi kuimarisha huduma za afya katika mataifa yetu. Benki ya CRDB itashirikiana nawe katika maeneo haya yote,” amesema Nsekela.

Kwa upande wake, Profesa Janabi ambaye ameimarisha ufanisi huduma hospitalini hapo tangu alipoteuliwa kuwa mkurugenzi mtendaji mwaka 2022, ameishukuru Benki ya CRDB kwa kwenda kumuaga akisema ni kampuni ya kwanza kufanya hivyo jambo linaloonyesha heshima kubwa ambayo  taasisi hiyo kubwa ya fedha imempa.

“Uhusiano wangu na Benki ya CRDB ni wa muda mrefu. Tangu nilipokuwa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) tulikuwa pamoja mkitusaidia kugharimia matibabu ya watoto. Nafurahi mmenikumbuka leo na kuja kuniaga,” amesema Profesa Janabi.

Akitarajiwa kuondoka wiki ijayo, Profesa Janabi anaiacha Tanzania akikumbukwa kwa utoaji wake wa elimu kupitia mitandao ya kijamii jambo lililoongeza hamasa ya kuepuka ulaji usiozingatia mahitaji ya kiafya unaoweza kumsababishia mtu magonjwa yasiyoambukiza.

Katika kuendeleza elimu hiyo, Profesa Janabi aliwaeleza wafanyakazi wa Benki ya CRDB kwamba wangepata chakula cha mchana pamoja na akasisitiza: “Mlo wetu leo utakuwa tunda moja la apple (tufaa).”

Akiwa mkurugenzi mtendaji mwanzilishi wa JKCI, Profesa Janabi alifanikiwa kuifanya kuwa taasisi mahiri inayohudumia wagonjwa wa ndani na watokao nje ya nchi hivyo kuacha mchango ambao hautosahaulika.

Balozi wa Akaunti ya Junior Jumbo, Paula Masanja aliwatia moyo wazazi waliojifungua watoto njiti na kuwahamasisha kuitumia akauniti hiyo kwa ajili ya watoto yao akisema ni muhimu kuwa na akiba kwa ajili ya matumizi yatakayojitokeza wakati wowote.
 
“Nami ni mzazi mwenye mtoto mdogo kama ninyi. Akaunti ya Junior Jumbo ni nzuri, itumieni kwa ajili ya watoto wenu,” alihamasisha Paula.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...