Na. Mwandishi Wetu, Zanzibar.

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Dkt. Jim Yonaz ameipongeza Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi kwa kukamilisha zoezi la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na kuendelea vyema na maandalizi ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.

 

Dkt. Yonazi ametoa pongezi hizo leo tarehe 09 Juni, 2025 Kisiwani Unguja, Zanzibar wakati wa kufungua kikao cha Baraza la Wafanyakazi la INEC,  ambapo imewaasa viongozi wa Tume kuendelea kuwa imara na kufanya kazi kwa bidii na ushirikiano ili kuhakikisha kuwa uchaguzi unakwenda vizuri.

 

“Kwanza niwapongeze sana kwa kukutekeleza jukumu hili kubwa ambalo mmekabidhiwa na Taifa letu na kwa namna ya pekee kabisa Mwenyekiti wa Baraza unifikishie salamu za pongezi kwa Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele pamoja na wajumbe wa Tume kwa kazi kubwa ambayo mmeifanya katika kuhakikisha kuwa shughuli za uchaguzi nchini kwetu zinakwenda vizuri,” amesema Dkt. Yonazi.

 

Ameeleza kuridhishwa na jinsi Tume ilivyotekeleza kwa ufanisi zoezi la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na kuongeza kuwa ni matarajio ya Serikali kuwa utendaji huo mzuri wa Tume utaendelea kwa viwango vya juu kwa mujibu wa katiba, sheria na taratibu mbalimbali ambazo zimewekwa.

 

Awali akimkaribisha mgeni rasmi, Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi ambaye pia ni Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Ndugu. Kailima Ramadhan amesema tayari Tume imekamilisha awamu ya kwanza ya uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura ambapo kwa sasa inaendelea na uboreshaji wa awamu ya pili.

 

“Tume imeshakamilisha uboreshaji wa awamu ya kwanza na imeshachakata na kutoa daftari la awali na imeshakamilisha uboreshaji wa awamu ya pili mzunguko wa kwanza na mzunguko wa pili. Tunategemea kuanzia tarehe 28 mwezi huu (tarehe 28 Juni, 2025) tutaanza mzunguko wa tatu wa uboreshaji katika Vyuo vya Mafunzo Tanzania Zanzibar na Magereza Tanzania Bara kwa wanafunzi na wafungwa waliohukumiwa kifungo chini ya miezi sita,” amesema Kailima.

 

Katibu huyo wa Baraza amesema mzunguko huo wa tatu utahusisha vituo 140 vya kuandikisha wapiga kura ambapo 130 vipo kwenye magereza Tanzania Bara na vituo 10 vipo kwenye vyuo vya mafunzo Tanzania Zanzibar. Zoezi hilo linatarajiwa kufanyika kwa siku saba hadi tarehe 04 Julai, 2025.

 

Ameongeza kuwa Tume imekamilisha maandalizi ya nyaraka mbalimbli kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025 ikiwa ni pamoja na Kanuni za Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani za Mwaka 2025, Kanuni za Maadili ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani za Mwaka 2025 na maelekezo mbalimbali kwa ajili ya watendaji wa uchaguzi na wadau wa uchaguzi kupata miongozo kwa ajili ya utekelezaji wa uchaguzi.

 

Alimkumbusha mgeni rasmi kuwa tayari Tume imekamilisha zoezi la ugawaji wa majimbo na kwamba kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2025 kutakuwa na jumla ya majimbo 272 yatakayofanya uchaguzi wa wabunge katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kata 3960 kwa ajili ya uchaguzi wa madiwani kwa Tanzania Bara.

 

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Dkt. Jim Yonaz (kushoto)  na Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi la Tume, Ramadhani Kailima,  pamoja na wajumbe wa baraza la Wafanyakazi la Tume wakiimba wimbo wa wafanyakazi wakati kabla ya kuanza kikao cha Baraza la Wafanyakazi  Mjini Unguja, Zanzibar leo Juni 9,2025. (Picha na INEC).  


Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Dkt. Jim Yonaz (kulia) akizungumza jambo na Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi la Tume, Ramadhani Kailima,  wakati Katibu Mkuu huyo alipofika kufungua Kikao cha Baraza la Wafanyakazi la Tume Mjini Unguja, Zanzibar leo Juni 9,2025. (Picha na INEC). 


Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...