Na: Calvin Edward Gwabara – Dar es Salaam.

Imebainishwa kuwa Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria nchini (OCPD) ndio nguzo muhimu inayoshikilia Uandishi, Urekebu na Ufasili wa sheria Kuu na sheria Ndogo nchini kwakuwa bila ofisi hiyo hakuna sheria ya nchi  inayokwenda kutungwa bungeni.

Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro akiangalia sehemu ya vitabu vilivyoandaliwa na OCPD kwaajili ya matumizi ya kazi za ufasili na urekebu.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro wakati akizungumza na Waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali vya habari nchini alipotembelea banda la OCPD kwenye maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya SABASABA yanayoendelea kwenye viwanja vya Mwl Julius Kambarage Nyerere jijini Dar es salaam.

“Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria nchini ni Ofisi muhimu sana katika mchakato mzima wa utunzi, Urekebu na Ufasili wa sheria za nchi, bila Ofisi hii hakuna sheria ambayo itakwenda bungeni kutungwa, bila ofisi hii hakuna sheria ambayo itafanyiwa Urekebu wala marekebisho lakini pia bila ofisi hii hakuna sheria ndogo ambayo itatungwa hivyo ni Ofisi muhimu sana katika mchakato mzima wa sheria nchini” Alifafanua Mhe. Dkt. Ndumbaro.

Aliongeza” Ikifa Ofisi hii maana yake Mahakama itapata shida katika utoaji wa haki maana ndiyo Ofisi ambayo inatuambia sheria sahihi ni ipi na ya toleo la mwaka fulani lakini pia sheria ipi si sahihi, lakini kwa sasa wanafanya kazi nzuri sana ya kufasili sheria zetu zote kutoka katika lugha ya Kiingereza kwenda katika lugha yetu ya Kiswahili”.

Amesema kwa taarifa alizonazo hadi kufikia tarehe 30 mwezi wa sita tayari OCPD ilikuwa imeshafanya ufasili wa sheria 300 kati ya sheria 446 na kwamba Serikali katika mwaka huu wa fedha wametenga fedha za kutosha kwa Ofisi hiyo ili iweze kukamilisha ufasili wa sheria zote za nchi Watanzania waweze kuzielewa.

Waziri huyo wa Katiba na Sheria amesema Ofisi hiyo ya Mwandishi Mkuu wa Sheria nchini ni Ofisi muhimu katika mchakato mzima wa uchakataji wa sheria za nchi na inasaidia Bunge kwenye kuchakata miswada kuwa sheria kamili zinazozingatia misingi yote muhimu ya utungwaji wa sheria.

Awali akitoa maelezo kwa Waziri bandani hapo Mwandishi wa sheria kutoka OCPD Bwana Philemon Mrosso amemueleza Waziri huyo kuwa Ofisi hiyo ipo kwenye hatua za mwisho za kukamilisha zoezi la ufasili wa sheria zilizobakia sambamba na kanuni zake ili ziweze kutoka kabla ya mwezi octoba mwaka huu kwa matumizi.

“Mhe. Waziri naomba nikujulishe kuwa ofisi yetu inashiriki maonesho haya kuweza kutoa elimu kwa watanzania na wadau wote wa sheria kuhusu mchato mzima wa utungwaji wa sheria lakini pia kuwafahamisha kuhusu majukumu ya Ofisi hii ili wanapohitaji msaada katika masuala yaliyo ndani ya mamlaka ya Ofisi yetu waweze kutufikia kirahisi na kupata msaada” Alieleza Mrosso.

Aidha ameongeza kuwa wanapokea maoni mbalimbali ya Wananchi na wadau kuhusu sheria za nchi na kuwaelekeza njia sahihi za kufikisha mawazo yao ikiwemo nafasi yao kama jamii katika utungwaji wa sheria za nchi katika maeneo mbalimbali kupitia wawakilishi wao ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mwandishi wa sheria kutoka OCPD Bwana Philemon Mrosso akimkabidhi zawadi Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Ndumbaro

Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro akisaini kitabu cha wageni wanaotembelea banda hilo la OCPD.

Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro akijisajili kidigitali kwenye mfumo maalumu wa wageni kwenye banda hilo.

Wanafunzi wakijisajili baada ya kupata maelezo na elimu kwenye banda la OCPD


Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...