Kampuni inayoongoza kwa huduma za usafiri mtandao nchini, Bolt, imekutana na waandishi wa habari katika mkutano maalum na wa kina kwa lengo la kutoa ufafanuzi kuhusu mfumo wa kamisheni na punguzo la nauli kwenye app yake, kufuatia maandamano ya hivi karibuni kutoka kwa baadhi ya madereva.
Akizungumza na vyombo vya habari, Dimmy Kanyankole, Meneja Mkuu wa Bolt Afrika Mashariki, alieleza kuwa madereva hawabebi gharama za punguzo wanazopewa abiria.
Alifafanua kuwa pale abiria anapopata punguzo la matangazo — kwa mfano punguzo la asilimia 40 — abiria hulipa kiasi kilichooneshwa kwenye programu, huku Bolt ikimrejeshea dereva sehemu ya fedha iliyopunguzwa mara baada ya safari kukamilika. Hii ina maana kuwa dereva hupokea mapato yake kamili ya safari husika, bila kuathiriwa na ofa yoyote inayoendelea.
“Madereva ni mhimili wa jukwaa letu. Uwezo wao wa kupata kipato cha uhakika na endelevu ni msingi wa mafanikio yetu ya muda mrefu. Tumejizatiti kuendesha mfumo wenye haki na uwazi, unaolinda mapato ya madereva huku ukihakikisha huduma inabaki nafuu kwa abiria,” alisema Kanyankole, akisisitiza kuwa uwazi ni nguzo kuu ya uendeshaji wa Bolt.
Kuhusu muundo wa kamisheni, kampuni ilieleza bayana kuwa inatoza kamisheni ya asilimia 20, kiwango kilicho ndani ya wigo wa asilimia 15 hadi 25 unaoruhusiwa na LATRA. Aidha, Bolt hutoza ada ya kuhifadhi safari (booking fee) ya asilimia 2 pekee, ambayo huoneshwa wazi kwenye risiti ya kila safari inayokamilika. Licha ya madai ya baadhi ya waandamanaji kuwa kamisheni imeongezwa, kampuni imethibitisha kuwa kiwango cha asilimia 20 kimekuwa kikitumika kwa miaka kadhaa sasa.
Mkutano huo ni sehemu ya juhudi za Bolt kuimarisha mawasiliano ya wazi na vyombo vya habari, madereva na wadau wa sekta kadri tasnia ya usafiri mtandao nchini inavyoendelea kukua.
Bolt imesisitiza dhamira yake ya kuendelea kuwa mshirika thabiti wa muda mrefu katika sekta ya usafiri nchini, kwa kuzingatia ukuaji wenye uwajibikaji, ulinganifu wa kikanuni na kuimarisha imani ya madereva kupitia uwazi na mawasiliano endelevu.



Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...