
NISHATI jadidifu pamoja na miundombinu ya maji inayojitegemea vinaendelea kubadilisha uendeshaji wa hospitali, vituo vya huduma za malazi na jamii za vijijini nchini Tanzania, huku taasisi zikilenga kupunguza utegemezi wa dizeli, kudhibiti changamoto za kuyumba kwa umeme wa gridi na kuimarisha uhakika wa huduma muhimu.
Wachambuzi wanaeleza kuwa mpito unaoendelea wa nishati nchini Tanzania unazidi kutawaliwa na mifumo ya miundombinu iliyogatuliwa, hasa katika sekta ambazo mwendelezo wa huduma hauwezi kutegemea tu kasi ya upanuzi wa gridi ya taifa.
Katika maeneo ambayo umeme usiokatika na maji safi ni muhimu, mifumo ya sola isiyounganishwa na gridi pamoja na miundombinu ya matibabu ya maji sasa inaingizwa katika mipango ya muda mrefu badala ya kuonekana kama suluhisho la muda.
Miongoni mwa kampuni zinazofanya kazi katika eneo hili ni Gadgetronix, ambapo miradi yake ya mwaka 2025 inaonesha kuongezeka kwa mwelekeo wa kuweka Sola katika hospitali, mifumo ya matibabu ya maji, pampu za maji za sola na miundombinu ya usambazaji maji vijijini.
Upatikanaji wa umeme wa uhakika bado ni changamoto kubwa kwa vituo vingi vya afya katika maeneo ya mbali, ambako vifaa vya upasuaji, maabara, uhifadhi wa chanjo na taa za dharura vinahitaji umeme endelevu.
Baada ya mchakato wa zabuni wa kikanda, Gadgetronix ilipewa kandarasi ya kubuni, kusambaza, kufunga na kutunza mifumo ya sola isiyounganishwa na gridi kwa vituo 17 vya afya vinavyohudumia kambi za wakimbizi za Nyarugusu na Nduta pamoja na jamii zinazozunguka katika wilaya za Kasulu na Kibondo.
Mradi huo unaunganisha uzalishaji wa sola na hifadhi ya betri za lithiamu ili kuhakikisha uendeshaji usiokatika bila kujali umbali na gridi ya taifa.
Ili kukabiliana na changamoto za usafirishaji katika maeneo ya mbali, vitengo vya sola vilivyowekwa kwenye makontena na vinavyoweza kusimikwa haraka vilitumika, hatua iliyoharakisha ufungaji na kupunguza muda wa ujenzi.
Mfumo huo pia unajumuisha taratibu za matengenezo na ufuatiliaji ili kudumisha upatikanaji wa huduma katika maeneo yaliyotawanyika kijiografia.
Wataalamu wa nishati wanasema mifumo ya sola kwa hospitali inayogatuliwa sasa inaonekana kama miundombinu ya msingi katika utoaji huduma za afya vijijini ambako uhakika wa gridi hubadilika badilika.
Akizungumzia vipaumbele vya usanifu wa mifumo hiyo, Mwanzilishi na Mtendaji Mkuu Hasnain Sajan alisema kipaumbele kikuu ni uhakika wa huduma: “Daktari anapoingia chumba cha upasuaji, vifaa lazima vifanye kazi. Chanjo zinapohifadhiwa, mnyororo wa baridi lazima udumu.”
Wachambuzi wanaona mwelekeo huu wa hospitali kutumia nishati jadidifu ukiakisi kuachana polepole na utegemezi wa jenereta za dizeli kuelekea uimara wa nishati uliobuniwa kitaalamu.
Zaidi ya sekta ya afya, mifumo ya maji inayotumia sola na vituo vya kisasa vya matibabu ya maji vinaongezeka kote Tanzania Bara na Zanzibar.
Zanzibar, visima vya Kizimbani na Weni vilibadilishwa kutoka pampu za dizeli kwenda sola, hatua iliyothabiti usambazaji wa kila siku na kuondoa gharama za mafuta.
Makadirio yanaonesha matumizi ya zaidi ya lita 33,000 za dizeli kwa mwaka yameondolewa, hivyo kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa.
Nchi nzima, zaidi ya pampu 600 za maji za sola na vitengo 400 vya usambazaji maji vinavyotumia sola vimesimikwa katika miradi ya kilimo, taasisi za umma na vituo vya maji vya jamii.
Mifumo ya matibabu ya maji inayoendeshwa na sola sasa inaunganishwa na miundombinu ya upampuji ili kuhakikisha ubora na usalama wa maji, hasa maeneo ambayo mitambo ya kawaida inayotumia gridi haiwezekani.
Wapangaji wa miundombinu wanasema mifumo ya maji inayotumia nishati jadidifu sasa inachukuliwa kama suluhisho la kudumu la utoaji huduma badala ya hatua za muda za kupunguza gharama.
Upanuzi huo umefika pia katika Kisiwa cha Pemba, ambako miradi mitano ya upampaji maji katika wilaya za Wete na Micheweni inaingizwa sola chini ya programu ya ustahimilivu inayofadhiliwa na Umoja wa Ulaya na kutekelezwa na Oikos East Africa. Mradi uliopatikana na Gadgetronix unahusisha usambazaji na usimikaji wa mifumo ya sola ya kupampu maji ili kuimarisha upatikanaji wa maji Kaskazini mwa Pemba.
Wataalamu wa maendeleo wanaeleza kuwa miundombinu ya maji visiwani hukabili changamoto za usafirishaji na mazingira kama chumvi nyingi, hivyo mifumo ya sola inaonekana kuwa uwekezaji wa kudumu unaopunguza gharama za uendeshaji kwa muda mrefu.
Kwa ushirikiano na taasisi za kifedha ikiwemo Tanzania Investment Bank na programu za maendeleo zinazoungwa mkono na World Bank, miundombinu ya usambazaji maji vijijini imepelekwa katika mikoa ya Mtwara, Tabora na Shinyanga.
Katika mfumo huu, vituo vya maji vya jamii vinawekewa teknolojia ya sola na mifumo janja ya usambazaji inayowawezesha wananchi kupata maji safi kwa malipo ya simu. Teknolojia hiyo inadhibiti usambazaji, inaongeza uwajibikaji wa mapato na kupunguza hatari za matumizi ya fedha taslimu.
Wataalamu wa maendeleo wanasema muunganiko wa mifumo ya maji inayotumia nishati jadidifu na malipo ya kidijitali unaongeza uendelevu wa miradi ya maji vijijini, hasa ambako changamoto za fedha za matengenezo na ukusanyaji mapato zilikuwa kubwa. Kwa kuunganisha upampuji wa sola, matibabu ya maji na miamala ya simu, miundombinu ya maji inayogatuliwa sasa inaendeshwa kama huduma endelevu za kijamii.

Ingawa afya na maji ndiyo msingi wa miradi ya hivi karibuni, mifumo ya nishati jadidifu imeenea pia katika maeneo ya utalii kama Serengeti, Ngorongoro Conservation Area, Tarangire na Lake Manyara, ambako uhakika wa umeme huathiri moja kwa moja uzoefu wa wageni na mwendelezo wa shughuli.
Wataalamu wa sekta hiyo wanasema usanifu wa mifumo ya umeme ndani ya maeneo yaliyohifadhiwa unahitaji uelewa wa kanuni za hifadhi, uratibu wa usafirishaji na mabadiliko ya mahitaji ya msimu. Timu za kiufundi zimewekwa kudumu Serengeti na Ngorongoro kutoa matengenezo ya haraka inapohitajika, huku baadhi ya miradi ya malazi ikiendeshwa chini ya mikataba maalum ya huduma yenye wahandisi wa ndani.
Kwa ujumla, ukubwa na usambazaji wa miradi ya nishati jadidifu na miundombinu janja ya maji vinaonesha kuwa mifumo iliyogatuliwa sasa inavuka hatua ya majaribio na kuwa sehemu ya msingi ya utoaji huduma nchini Tanzania. Kadri gharama za dizeli zinavyoongezeka na uthabiti wa gridi kubaki changamoto katika maeneo ya mbali, hospitali na mifumo ya maji inayotumia nishati jadidifu inazidi kuchukuliwa kama rasilimali kuu za huduma badala ya nyongeza za hiari, huku hatua inayofuata ikitegemea zaidi uaminifu wa uendeshaji kwa muda mrefu.


.jpg%20(1).jpeg)
.jpeg)
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...