Puma Energy Tanzania imezindua rasmi Kituo Mama cha Gesi Asilia Iliyoshindiliwa (CNG) kilicho kikubwa na cha kisasa zaidi barani Afrika.
Kituo hicho cha kihistoria kimezinduliwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, tukio linaloashiria hatua kubwa katika safari ya Tanzania kuelekea matumizi ya nishati safi, nafuu na ya uhakika.
Kikiwa jijini Dar es Salaam, kituo hiki cha kisasa kimeundwa kukidhi ongezeko la mahitaji ya CNG, ambayo ni mbadala nafuu na rafiki kwa mazingira badala ya mafuta ya petroli na dizeli.
Kituo hicho kitahudumia magari madogo, mabasi, na malori makubwa, huku kikifanya kazi kama kitovu cha usambazaji wa gesi kwenda vituo vingine vidogo vya CNG nchini kupitia trela maalum za kusafirisha gesi (tube-trailers).
“Kituo hiki Mama cha CNG ni zaidi ya miundombinu; ni ishara ya imani yetu ya muda mrefu kwa Tanzania na dhamira yetu ya kuleta thamani kwa pamoja. Tunajivunia kushirikiana na Serikali kutekeleza mradi utakaoliendesha taifa mbele kwa miaka mingi ijayo,” alisema Bi. Fatma Abdallah, Mkurugenzi Mtendaji wa Puma Energy Tanzania.
Kituo hiki kipya kina uwezo wa kuhudumia aina mbalimbali za vyombo vya usafiri, ikiwemo magari madogo, mabasi na malori makubwa. Aidha, kitafanya kazi kama kitovu kikuu cha kusambaza CNG kwa vituo vingine vidogo nchini kupitia trela maalum za gesi.
Akizungumza katika hafla ya uzinduzi, Waziri Mkuu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba ameusifu mradi huo kuwa mfano thabiti wa mafanikio ya mkakati wa Serikali ya Awamu ya Sita katika kuimarisha mazingira bora ya uwekezaji na kutumia ubia kati ya Serikali na sekta binafsi (PPP) kwa maendeleo ya Taifa.
“Puma Energy Tanzania ni mfano mzuri wa mafanikio ya ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi, ikitoa huduma bora za nishati huku ikichangia mapato ya Serikali, ajira, na ujenzi wa miundombinu ya kimkakati.
Uwekezaji huu unaonyesha dhamira ya Serikali ya kuendelea kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji huu unaendana kikamilifu na vipaumbele vyetu vya kitaifa,” alisema Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, aliunga mkono kauli hizo akibainisha kuwa muundo wa kipekee wa umiliki wa kampuni hiyo unahakikisha mafanikio ya kibiashara yanatafsiriwa moja kwa moja kuwa manufaa ya Taifa.
“Ubia huu unaonyesha kuwa kuunganisha ushiriki wa Serikali na ufanisi wa sekta binafsi kunaleta miundombinu muhimu na faida kubwa za kifedha kwa Watanzania,” alisema Bw. Mchechu.
Katika kipindi cha ujenzi wa mradi huu, zaidi ya ajira 300 zilitolewa kwa Watanzania pekee, ikiwemo nafasi 100 za kitaalamu kwa wahandisi na mafundi.
Mradi pia uliwapa kipaumbele wakandarasi wa ndani na biashara ndogo na za kati (SMEs), na hivyo kuingiza mtaji mkubwa katika uchumi wa eneo husika. Kituo hiki kinapoanza kufanya kazi kikamilifu, kitaendelea kutoa ajira za kudumu na kuwezesha uhamishaji muhimu wa ujuzi katika sekta ya gesi asilia inayokua kwa kasi.
“Uwekezaji huu ni sehemu ya dhamira ya muda mrefu ya Puma Energy nchini Tanzania.” alisema Wakili Emmanuel G. Bakilana, Mkuu wa Idara ya Sheria na Mahusiano ya Puma Energy Tanzania.
Katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita, kampuni imelipa zaidi ya shilingi trilioni 1.4 kama kodi na ushuru mbalimbali. Mwaka 2025, kampuni ilitangaza gawio la shilingi bilioni 21 kwa wanahisa.
Rekodi hii ya uwajibikaji na uwazi ilitambuliwa hivi karibuni kwa tuzo mbalimbali kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
Hafla ya uzinduzi ilihudhuriwa na viongozi waandamizi wakiwemo Waziri wa Nishati, maafisa wa Serikali, na wawakilishi wa taasisi muhimu za udhibiti kama EWURA, TPDC na TANESCO, jambo lililoonesha ushirikiano mpana uliowezesha kufikiwa kwa hatua hii muhimu ya kitaifa.







Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...