Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.), amekutana na kumuaga Balozi mteule wa Tanzania nchini Comoro, Mhe. Salim Othman Hamad, katika kikao kilichofanyika katika ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.
Katika kikao hicho, Waziri Kombo amemtaka Balozi Hamad kutumia ipasavyo diplomasia ya uchumi ili kuimarisha mahusiano ya kibiashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Comoro, pamoja na kukuza sekta ya utalii. Akisisitiza umuhimu wa kutumia nafasi hiyo kuibua fursa mpya za kiuchumi zitakazowanufaisha wananchi wa pande zote mbili.
Vilevile, Waziri Kombo amesisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano wa kidiplomasia uliopo kati ya Tanzania na Comoro, akihimiza uwakilishi madhubuti unaolenga kulinda na kukuza maslahi ya Taifa.
Kwa upande wake, Mhe. Hamad amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan, kwa imani na dhamana aliyompa ya kuiwakilisha nchi, na kuahidi kuitumikia Tanzania kwa weledi na uadilifu.
Kabla ya uteuzi wake, Mhe. Hamad alikuwa Mshauri wa Rais anayeshughulikia masuala ya siasa.





Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...