Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Dkt. John Mduma, amesema kuwa ushirikiano kati ya WCF na Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) utasaidia kupunguza ajali za barabarani na kulinda nguvu kazi ya Taifa.Akizungumza katika hafla ya utiaji saini wa mkataba wa ushirikiano (MoU) iliyofanyika tarehe 31 Machi 2026 jijini Dar es Salaam, Dkt. Mduma alisema kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kuimarisha usalama barabarani pamoja na kuongeza uelewa kwa madereva ambao ni wadau wakuu wa Mfuko huo.

“Ushirikiano huu utatuwezesha kuimarisha usalama barabarani na kuongeza uelewa kwa madereva, ambao ni sehemu muhimu ya wadau wetu,” alisema Dkt. Mduma.

Alieleza kuwa WCF ilianzishwa kwa lengo la kushughulikia fidia kwa wafanyakazi wanaopata ajali au magonjwa yatokanayo na kazi, lakini tathmini zinaonesha kuwa sehemu kubwa ya madai yanatokana na ajali za barabarani, hali inayohitaji juhudi za pamoja kupambana nayo.

“Sehemu kubwa ya madai tunayopokea yanatokana na ajali za barabarani, hivyo kuna umuhimu wa wadau kushirikiana kupunguza tatizo hili,” aliongeza.
Akizungumza zaidi, Dkt. Mduma alisema kuwa kupitia mkataba huo, taasisi hizo mbili zitashirikiana katika maeneo muhimu ikiwemo utoaji wa mafunzo na elimu kuhusu usalama wa usafirishaji, kufanya tafiti, kubadilishana taarifa pamoja na kujengeana uwezo wa kitaalamu.

“Makubaliano haya yatajikita katika mafunzo, tafiti, ubadilishanaji wa taarifa na kujengeana uwezo wa kitaalamu ili kuongeza ufanisi katika utendaji kazi,” alisema.

Aidha, alibainisha kuwa ushirikiano huo utaongeza tija na ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya kila taasisi na kusaidia kufikia malengo ya pamoja ya kupunguza ajali pamoja na kuboresha ustawi wa wafanyakazi.
Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji, Mhandisi Dkt. Prosper Mgaya, pamoja na wadau mbalimbali wa sekta ya usafirishaji waliokuwepo, walishuhudia utiaji saini wa makubaliano hayo ambayo yanatarajiwa kuleta mageuzi chanya katika sekta ya usafirishaji nchini.

Hafla hiyo ilihudhuriwa pia na wawakilishi kutoka taasisi mbalimbali zikiwemo LATRA, Jeshi la Polisi Kitengo cha Usalama Barabarani, TANROADS, TARURA, pamoja na vyama vya wamiliki wa mabasi na malori.



 

Mbeya- Jumanne, Machi 31, 2026


Katika kuadhimisha miaka 25 ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), Kampasi ya Mbeya imefanya shughuli za kijamii, ikiwemo kutembelea na kutoa misaada kwa vituo viwili vya watoto yatima jijini Mbeya.

Shughuli hiyo imehusisha watumishi wa chuo hicho wakiongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Mhe. Solomon Itunda, pamoja na Mkurugenzi wa Kampasi ya Mbeya, Ndugu Saidy Nzagamba. Vituo vilivyotembelewa ni Kituo cha Watoto Yatima Iwambi kilichopo mtaa wa Iwambi na Kituo cha Bi Aisha Foundation kilichopo mtaa wa Soweto.

Katika ziara hiyo, TPSC Kampasi ya Mbeya imekabidhi mahitaji mbalimbali kwa ajili ya watoto hao, yakiwemo mchele, maharage, sabuni, juisi, mafuta ya kupikia, vitunguu, na mbuzi kwa ajili ya lishe na mahitaji ya kila siku.

Akizungumza wakati wa kukabidhi zawadi hizo, Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Mhe. Itunda, aliipongeza TPSC kwa maadhimisho yenye dhamira ya kugusa maisha ya watu. Alisema hatua hiyo inaonyesha utu na maadili ya utumishi wa umma yanayojengwa na chuo hicho.

"Chuo hiki kimeendelea kuwa chachu ya maendeleo kwa taifa letu kwa kutoa watumishi bora. Kila kinachofanywa hapa kinaonyesha dhamira ya kweli ya kuwahudumia wananchi na kujenga jamii yenye mshikamano," alisema Mhe. Itanda.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Kampasi ya Mbeya, Ndugu Saidy Nzagamba, alisema chuo hicho kimeamua kushiriki na kusaidia watoto yatima kama sehemu ya kuwajengea faraja na kuwahakikishia kuwa jamii inawajali.

"Tunatambua changamoto wanazokabiliana nazo watoto hawa, ndiyo maana tumeamua kuwa jirani nao na kuwagusa kwa upendo. Huu ni mwanzo wa dhamira yetu kuendelea kushiriki shughuli za kijamii katika siku zijazo," alisema Nzagamba.

Viongozi wa vituo vya Iwambi na Bi Aisha Foundation waliushukuru uongozi wa TPSC Kampasi ya Mbeya kwa upendo na michango iliyotolewa, wakisema misaada hiyo itasaidia kwa kiasi kikubwa katika malezi na ustawi wa watoto.





















Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) iliyopo jijini Dodoma, inatarajia kuhitimisha rasmi maadhimisho ya miaka 10 tangu kuanzishwa kwake kwa kufanya harambee maalum ya kuchangisha fedha kwa ajili ya matibabu ya upandikizaji uloto na figo kwa wananchi wenye uhitaji.

Akizungumza na waandishi wa habari, Mkurugenzi Mtendaji wa hospitali hiyo, Profesa Abel Makubi, amesema kuwa maadhimisho hayo yalianza Oktoba 13, 2025, na yatahitimishwa Mei 8, 2026, baada ya kudumu kwa takribani miezi saba.

Prof. Makubi amesema kuwa lengo kuu la maadhimisho hayo ni kuhamasisha wadau kushiriki katika harambee itakayolenga kukusanya shilingi bilioni 7 ndani ya kipindi cha miaka miwili. Fedha hizo zitatumika kusaidia matibabu ya wagonjwa 100, ambapo 50 ni watoto wenye ugonjwa wa selimundu wanaohitaji upandikizaji wa uloto, na wengine 50 ni wagonjwa wa figo.

Ameeleza kuwa gharama za matibabu hayo ni kubwa, hivyo hospitali imeona umuhimu wa kushirikiana na wadau mbalimbali wakiwemo Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) pamoja na taasisi nyingine ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma hizo muhimu.

Kwa mujibu wa Prof. Makubi, hospitali hiyo kwa sasa inahudumia takribani wananchi milioni 10 kutoka mikoa nane ya Tanzania, na imeanza pia kupokea wagonjwa kutoka nje ya nchi kama sehemu ya kukuza utalii wa matibabu.

Ameongeza kuwa hospitali hiyo ina jumla ya watumishi 1,173, wakiwemo madaktari bingwa zaidi ya 100, na kwa sasa inatoa huduma 20 za kibingwa pamoja na huduma 18 za ubingwa bobezi.

Katika hatua nyingine, Prof. Makubi amesema BMH ina mipango ya kuanzisha miradi ya kimkakati ikiwemo vituo vya umahiri katika matibabu ya saratani, upanuzi wa huduma za upandikizaji uloto, pamoja na kuanzisha taasisi maalum za macho, moyo, na upasuaji wa ubongo na mifupa ndani ya miaka mitano ijayo.

Amesema lengo ni kuifanya hospitali hiyo kuwa kitovu cha utalii wa matibabu nchini na barani Afrika.

Katika kilele cha maadhimisho hayo, mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan.

Sambamba na hilo, hospitali imepanga kufanya kongamano la kisayansi Mei 6, 2026, litakalowakutanisha wataalam wa afya, hususan katika masuala ya upandikizaji wa viungo.

Prof. Makubi ametoa wito kwa taasisi za afya, wadau wa maendeleo na wafadhili kujitokeza kwa wingi kuunga mkono juhudi hizo ili kusaidia kuokoa maisha ya wananchi wenye uhitaji wa matibabu hayo ghali.

BMH Kuadhimisha Miaka 10 kwa Harambee ya Bilioni 7 Kuboresha Huduma za Upandikizaji Uloto na Figo



 

 ✅Watoa Msaada kwa Makundi Maalum


  📍Hombolo, Dodoma.

Watumishi wa Wizara ya Madini leo Machi 31, 2026, wamepeleka tabasamu kwa jamii yenye uhitaji maalumu kwa kwa watoto yatima na wazee wasiojiweza wa Kituo cha Watoto cha Huruma kilichopo Hombolo, kinachoendeshwa na Masista wa Shirika la Mtakatifu Theresia.

Akikabidhi misaada hiyo  Kwa niaba ya Watumishi wa Wizara ya Madini Makao Makuu, Mkurugenzi Msaidizi wa Utawala kutoka Wizara ya Madini, Bi. Beatrice Matemu, ambaye alikua kiongozi wa msafara amesema kuwa hatua hiyo ni sehemu ya dhamira ya watumishi wa wizara hiyo kutoa kwa jamii sehemu ya kile wanachopata, hususan kwa makundi yenye uhitaji maalum kuelekea Sikukuu ya Pasaka.

Kwa upande wake, msimamizi wa kituo hicho, Sista M. Judy Claris, amesema kwa sasa kituo kinahudumia watoto 29 wenye umri wa kati ya miezi miwili hadi miaka minne na nusu, wanawake 27 pamoja na wanaume 25 wenye changamoto mbalimbali zinazohitaji uangalizi wa karibu na huduma endelevu.

Ameeleza kuwa pamoja na kulea na kuhudumia makundi hayo katika kituo hicho, wao pia hutoa misaada kwa jamii inayowazunguka, ambapo kila siku ya Jumanne hugawa vyakula kama mboga, unga na sukari, pamoja na kupika chakula kwa wahitaji wanaofika kituoni hapo.

Sista Judy ametoa wito kwa wadau na watu wengine kujitokeza kusaidia kituo hicho ili kiweze kuendelea kutoa huduma, akibainisha kuwa kwa sasa wanategemea zaidi shughuli ndogo za kilimo cha mbogamboga, njugu na maharage, pamoja na ufugaji wa ng’ombe kama chanzo cha kujikimu.

Katika ziara hiyo, watumishi wa Wizara ya Madini walikabidhi msaada uliojumuisha mahitaji muhimu ya kila siku kama mchele, unga, sabuni, unga wa lishe, taulo za kike, mafuta ya kupikia, chumvi, juisi na biskuti kwa ajili ya watoto.

Aidha, imeelezwa kuwa makundi hayo yanahitaji kwa kiasi kikubwa mahitaji ya msingi ya maisha ya binadamu ikiwemo chakula, mavazi, malazi pamoja na huduma za afya na dawa wanapougua.

Ziara hiyo imeacha alama ya faraja kwa wahitaji wa kituo hicho, huku ikisisitiza umuhimu wa mshikamano na upendo katika kujenga jamii inayojali na kuthamini utu wa kila mmoja.


 


*Ni ujenzi uliogharimu Sh.bilioni 25,changamoto ya kukatika umeme imebaki historia 

Na Said Mwishehe,Michuzi TV-Ifakara

MRADI wa ujenzi wa Kituo cha kupoza umeme cha Ifakara ambacho kimejengwa na Serikali kupitia Wakala wa Umeme Vijijini(REA) kwa gharama ya Sh.bilioni 25 kimewezesha kumaliza changamoto ya kukatika umeme mara kwa mara katika Wilaya ya Kilombero mkoani Morogoro.

Kwa sasa kituo hicho kinazalisha umeme wa megawati 18 na kati hizo ambazo zinatimika ni megawati 7 na hivyo kuwa na ziada ya megawati 11 ambapo wananchi,taasisi za umma na binafsi zimeondokana kabisa na umeme wenye mashaka.

Umeme wa uhakika ambao REA wameufanikisha kupitia kituo hicho ambacho no moja ya kituo kikubwa cha kupoza na kuzalisha umeme kujengwa na wakala huo kimewafanya wananchi wa Wilaya hiyo wapato milioni moja kumshukuru Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kwa kumaliza changamoto ya umeme katika Wilaya hiyo.

Akizungumza mbele ya Wahariri ambao ni Wanachama wa Jukwaa la Wahariri Tanzania(TEF) walioko katika ziara ya kutembelea miradi ya REA, Mkuu wa Wilaya ya Kilombero Dunstan Kyoba, amesema kituo hicho kimeondoa changamoto ya kukatika kwa umeme na kazi iloyobakia kwa sasa ni kuhamasisha watu kwenda kuwekeza kwani umeme ni wa uhakika.

Amesema kabla ya kujengwa kwa kituo hicho wananchi kwa muda mrefu walikuwa wakiteseka kwa umeme kuwa wa kukatikatikq lakini Rais Dk.Samia kwa maelekezo yake aliielekeza REA kujenga kituo hicho ambacho kimegharimu Sh.bilioni 25 hatua ambayo imewezesha kuwa na umeme wa uhakika.

“Serikali chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ilitoa takribani shilingi bilioni 25 kugharamia ujenzi wa kituo hicho, hatua iliyoongeza upatikanaji wa umeme kutoka megawati 3 hadi megawati 7 pamoja na sasa kuwepo kwa ziada ya megawati 11.

“Upatikanaji wa umeme wa uhakika umefungua fursa za uwekezaji katika sekta mbalimbali ikiwemo viwanda, kilimo, hoteli na huduma za afya,” amesema na kusisitiza kwa kazi nzuri ya REA katika Wilaya hiyo hivi sasa wametoa ombi kituo hicho kiitwe kituo cha kupoza umeme cha Samia kama sehemu ya kutambua jitihada zake katika kuhakikisha wananchi wanakuwa na umeme wa uhakika.

Hata hivyo ametoa rai kwa  wawekezaji kuwekeza katika Wilaya ya Kilombero na ukanda wa Morogoro Kusini unaojumuisha wilaya za Kilombero, Ulanga na Malinyi huku akiweka wazi Wilaya hiyo imebarikiwa kuwa na kila aina ya fursa ikiongozwa na kilimo pamoja na utalii.

Awali Meneja wa Usimamizi wa Miradi kutoka REA, Mhandisi Deogratius Nagu, amesema mradi huo umegharimu takribani Sh. bilioni 25, ukihusisha pia ujenzi wa njia za kusafirisha umeme za msongo wa kilovolti 33 zenye urefu wa kilometa 70 pamoja na huduma za ushauri elekezi.

“Ujenzi wa Kituo hiki umetumia teknolojia ya kosasa kutoka mataifa matatu ikiwemo transfoma kutoka Bulgaria, mifumo ya udhibiti na ulinzi kutoka Hispania pamoja na mifumo ya switching kutoka Ujerumani,”amesema Mhandisi Nagu alipokuwa akitoa taarifa ya kituo hicho kwa wahariri hao wakiongozwa na Mwenyekiti wa TEF Deodatus Balile.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa TEF, Balile ametoa pongezi kwa REA kwa kazi kubwa wanayofanya nchini ya kuhakikisha nchi inakuwa na umeme wa uhakika na Kamba kituo hicho cha kupoza umeme Ifakara unaonesha matumizi sahihi ya rasilimali za umma na mchango wa REA katika kusambaza umeme vijijini.

Balile ameongeza kwamba ongezeko la matumizi ya umeme hadi kufikia megawati saba ni ishara ya ukuaji wa shughuli za kiuchumi na maendeleo ya taifa kwa ujumla.

Katika hatua nyingine Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Kilimo Ifakara, Setina Ngailo, amesema shule yao ni moja ya wanafuika wa umeme wa REA na awali walikumbwa na changamoto ya kukatika kwa umeme hasa kipindi cha masika, hali iliyokuwa ikiathiri upatikanaji wa maji na mwanga shuleni.

“Kwa sasa changamoto hiyo imeondoka kabisa na tunapata huduma ya umeme muda wote.Umeme wa uhakika umewezesha wanafunzi kusoma bila kupata usumbufu ya kukosa umeme 

Wakati huo huo Msimamizi wa Hospitali ya Kansa ya Good Samaritan, Father Charles Masawe, amesema hapo awali walilazimika kutumia jenereta kutokana na umeme mdogo, hali iliyokuwa inaongeza gharama za uendeshaji.“Kwa sasa tunaendesha vifaa tiba kwa ufanisi zaidi kutokana na upatikanaji wa umeme wa uhakika,” alisema.

Kwa upande wake Meneja wa Kiwanda cha Kukoboa Mpunga cha Bezelengule, Enos Machumu, amesema uzalishaji umeongezeka kutoka tani 3 hadi tani 22 kwa siku kufuatia kuimarika kwa huduma ya umeme, huku pia wateja waliokuwa wameondoka wakirejea.







 Na. Joseph Mahumi, WF, Dar es Salaam


Serikali ya Tanzania imewakaribisha wawekezaji kutoka Uturuki kuwekeza katika sekta za kimkakati zikiwemo miundombinu, nishati na kilimo, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuharakisha maendeleo ya uchumi na kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.

Wito huo umetolewa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), wakati alipokutana na Balozi wa Uturuki nchini, Mhe. Dkt. Bekir Gezer, akiambatana na ujumbe kutoka Benki ya EXIM ya Uturuki, katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam.
 
Alitoa wito wa Uturuki kushiriki katika ujenzi wa miundombinu ya usafirishaji hususan katika ujenzi wa vipande vya Lot 3 na Lot 4 vya Reli ya Kisasa (Standard Gauge Railway (SGR)), ambavyo Benki ya EXIM ya Uturuki imeonesha nia ya kufadhili, ikiwa ni vipande muhimu katika kuunganisha mtandao wa reli unaoendelea kujengwa kutoka Dar es Salaam kuelekea maeneo ya ndani ya nchi na nchi jirani, vitakavyo chochea biashara ya kikanda na kimataifa.

“Kukamilika kwa mradi huu wa SGR, kutaiwezesha Tanzania kuwa kitovu cha usafirishaji na biashara katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, na utafungua fursa za uwekezaji katika maeneo yanayozunguka reli hiyo na kuunda korido ya maendeleo ya kiuchumi” alisema Mhe. Balozi Omar

Aliongeza kuwa Katika sekta ya nishati, Tanzania imepiga hatua kubwa kwa kuongeza uzalishaji wa umeme kutoka megawati 1,700 hadi zaidi ya megawati 4,000 ndani ya kipindi cha miaka michache iliyopita, kufuatia kukamilika kwa mradi wa Julius Nyerere Hydropower Project na Serikali inalenga kuongeza uzalishaji huo hadi kufikia megawati 8,000 ifikapo mwaka 2030, na hatimaye megawati 15,000 na kutoa wito wa uwekezaji zaidi kutoka Uturuki ikiwemo Exim Bank kupitia mfumo wa ubia kati ya sekta ya umma na binafsi (PPP).

Kwa upande wa kilimo, Mhe. Balozi Omar alieleza kuwa Tanzania ina fursa kubwa kutokana na rasilimali zake za ardhi yenye rutuba na vyanzo vya maji, na inaweza kujifunza kupitia uzoefu wa Uturuki katika kubadilisha sekta hiyo kutoka uzalishaji wa kawaida hadi wa kisasa unaotumia teknolojia za kisasa na kuisaidia Tanzania kufikia lengo la kuwa ghala la chakula barani Afrika.

Kwa Upande wake Balozi wa Uturuki nchini Tanzania, Mhe. Dkt. Bekir Gezer, alisema kuwa Tanzania na Uturuki ni nchi ndugu zenye uhusiano wa muda mrefu uliojengwa juu ya misingi ya kuaminiana, urafiki, mshikamano na kuheshimiana.

Mhe. Dkt. Gezer, alisema kuwa Tanzania ina umuhimu mkubwa kutokana na utulivu wake wa kisiasa na kiuchumi pamoja na wingi wa rasilimali za asili, na eneo la kijiografia la linaifanya kuwa kitovu muhimu cha biashara na usafirishaji, hali inayovutia si tu Uturuki bali pia mataifa mengine duniani kiuwekezaji.

Aliongeza kuwa kupitia taasisi kama Benki ya EXIM ya Uturuki na kampuni zake, nchi hiyo iko tayari kuendelea kushirikiana na Tanzania katika miradi ya maendeleo kwa manufaa ya pamoja.

Kikao hicho pia kilihudhuriwa na Kamishna wa Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Japhet Justine, Kamishna Msaidizi wa Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha, Bi. Tiba Kisonga, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Ellen Mahudu, Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Standard Chartered, Bw. Herman Kasekende, Mkurugenzi wa Fedha za Miradi na Uhusiano ya Kimataifa wa Benki ya EXIM ya Uturuki, Bi. Hatice Ürkmez, na maafisa wengine waandamizi wa Wizara ya Fedha na Benki ya EXIM ya Uturuki.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (kushoto), akiagana na Balozi wa Uturuki nchini Tanzania, Mhe. Dkt. Bekir Gezer, baada ya kukutana na kufanya mazungumzo katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, ambapo walijadili masuala ya ushirikiano ikiwemo kukuza uwekezaji katika sekta za kimkakati zikiwemo miundombinu, nishati na kilimo, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuharakisha maendeleo ya uchumi na kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akizungumza katika kikao chake na Balozi wa Uturuki nchini Tanzania, Mhe. Dkt. Bekir Gezer (hayupo pichani) aliyembatana na ujumbe kutoka Benki ya EXIM ya Uturuki, katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, ambapo aliwakaribisha wawekezaji  kutoka Uturuki kuwekeza katika sekta za kimkakati zikiwemo miundombinu, nishati na kilimo, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuharakisha maendeleo ya uchumi na kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.
Balozi wa Uturuki nchini Tanzania, Mhe. Dkt. Bekir Gezer, akizungumza jambo wakati wa kikao chake na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, ambapo walijadili masuala ya ushirikiano ikiwemo kukuza uwekezaji katika sekta za kimkakati zikiwemo miundombinu, nishati na kilimo, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuharakisha maendeleo ya uchumi na kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.
Baadhi ya Wajumbe kutoka Benki ya EXIM ya Uturuki walioambata na Balozi wa Uturuki nchini Tanzania, Mhe. Dkt. Bekir Gezer (hayupo pichani), wakimsikiliza Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), wakati wa kikao chao katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, ambapo walijadili masuala ya ushirikiano ikiwemo kukuza uwekezaji katika sekta za kimkakati zikiwemo miundombinu, nishati na kilimo, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuharakisha maendeleo ya uchumi na kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akiwa na wataalamu waandamizi wa Wizara ya Fedha na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, wakimsikiliza Balozi wa Uturuki nchini Tanzania, Mhe. Dkt. Bekir Gezer (hayupo pichani), aliyembatana na ujumbe kutoka Benki ya EXIM ya Uturuki, katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, ambapo aliwakaribisha wawekezaji kutoka Uturuki kuwekeza katika sekta za kimkakati zikiwemo miundombinu, nishati na kilimo, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuharakisha maendeleo ya uchumi na kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (Katikati mstari wa mbele), Balozi wa Uturuki nchini Tanzania, Mhe. Dkt. Bekir Gezer (wa pili kushoto mastri wa mbele), na viongozi wengine waandamizi kutoka Wizara ya Fedha, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Benki ya EXIM ya Uturuki na Benki ya Standard Chartered, wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kikao chao kilichofanyika Ofisi Ndogo za Wizra ya Fedha, Jijini Dar es Salaam, kilichojadili masuala ya ushirikiano ikiwemo kukuza uwekezaji katika sekta za kimkakati zikiwemo miundombinu, nishati na kilimo, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuharakisha maendeleo ya uchumi na kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Dar es Salaam)

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema aliyekuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) na Mbunge wa Isimani, Mheshimiwa William Lukuvi atakumbukwa kwa mengi na Watanzania kutokana na utumishi wake uliotukuka katika nafasi mbalimbali alizohudumu.

“Mheshimiwa Lukuvi atakumbukwa kwa mengi na Watanzania kutokana na utumishi wake uliotukuka katika nafasi mbalimbali. Mchango wake kwa Jamii na Watanzania kwa ujumla katika nafasi mbalimbali alizotumikia kuanzia Chama, Jimboni na Serikalini umekuwa chachu katika kuleta maendeleo kwa wananchi,” amesema Waziri Mkuu ambaye ameongoza mazishi hayo kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,  Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Jumanne, Machi 31, 2026) wakati akizungumza katika ibada ya mazishi ya marehemu iliyofanyika nyumbani kwake kwenye kijiji cha Idodi, wilayani Iringa, mkoani Iringa.

"Kwa niaba ya Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan nitumie nafasi hii kuwahahikishia kwamba jinsi alivyokuwa pamoja nanyi wakati wa uhai wake, na yale yaliyokuwa ndoto yake, yataendelea kutimizwa.

"Ni vema tukizingatia na kuyaishia yale tuliyoelezwa na viongozi wa dini pamoja na kwenye wasifu wake. Alikuwa akisisitiza ushirikiano baina ya Bunge na Mawaziri, leo hii tuyaenzi yote aliyoyasimamia."

Na kwa wana-Isimani, ninawasihi tuendelee kumuenzi, tusianze mashindano, tulinde heshima ya Mzee wetu kwa kuwa na staha."

Amesema Mheshimiwa Lukuvi alikuwa anajali maisha ya wale anaowaongoza na ndiyo maana ameweza kudumu jimboni kwa miaka 31. "Sisi wanasiasa tunajua, siyo kazi rahisi kuongoza kwa muda wote huo, lakini yeye aliweza kwa sababu aliweka kipaumbele  chake kwenye maisha ya wale anaowaongoza."

Amesema Serikali itaendelea kumuenzi kwa kuendelea kutekeleza miradi aliyoiacha hasa wa barabara ya lami ambayo alikuwa anaifuatilia sana. "Miradi ya Pawaga na Isimani yote itakamilishwa. Niwahakikishie kuwa Serikali itaendelea kuitekeleza kama sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya CCM lakini pia sehemu ya kumuenzi Mheshimiwa Lukuvi," amesema. 

Naye Spika wa Bunge la Tanzania, Mussa Azzan Zungu alisema kifo cha Mhe. Lukuvi kimeacha majonzi kwa kila mmoja na kwa uzito wa msiba huo,  Bunge limewakilishwa na wabunge 160.

"Mheshimiwa Lukuvi alikuwa anaujua uwezo wake na kifo chake ni pigo ambalo Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limepata kwa kuukosa umahiri wake Bungeni.

Mapema, Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara, Stephen Wasira alitumia fursa hiyo kuwaasa vijana wa CCM wajifunze na waige mapito ya Mhe. Lukuvi ambaye alianzia ngazi za chini kabisa hadi akafika kwenye uongozi wa Taifa.

"Mwaka 1974 alijiunga na chama cha TANU, akajiendeleza hadi kufikia nafasi ya Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana."

Alisema jambo kubwa la kujifunza kutoka kwa Mhe. Lukuvi ni jinsi alivyoweza kulea jimbo ilhali ana majukumu makubwa ya kitaifa. "Siyo wengi ambao anakuwa Mbunge au Waziri halafu analea jimbo. Watu aina hii wako wachache sana. Wengi wakipata vyeo wanasahau majimbo na kuja kuwaona wapigakura wakati wa uchaguzi," alisema na kushangiliwa. 

Alisema kuweza kudumu kwenye madaraka na Marais wanne tangu awamu ya Rais Mkapa hadi sasa, ni ishara tosha kwamba aliaminiwa na kuna jambo la kujifunza kutoka kwake. "Marais wote hawa walikuwa na watu wao, lakini kwa kuendelea kuwa naye, ina maana alikuwa na sifa na uwezo."

Ibada ya mazishi iliongozwa na Naibu Askofu wa Jimbo Katoliki la Iringa, Padre Paul Msombe ambaye alisisitiza kuwa ni vema kwatu wakaishi huku wakijiandaa kwa maisha ya baadaye mbinguni.

Akimzungumzia marehemu Lukuvi, Padre Msombe alisema: “Licha ya vyeo vyake alikuwa na unyenyekevu na mwenye kushirikiana na waumini wenzake. Tukumbuke kwamba ipo siku tutalala usingizi kama ndugu yetu William alivyolala usingizi wa amani. Kitu cha msingi ni kujiweka mikononi mwa Mungu, tufe katika BWANA. Hili ni suala la kila mmoja kujitazama na kujihoji kwamba mimi Mungu akiniita sasa hivi, ninaweza kusema nina haki ya kuingia mbinguni.?”

Mheshimiwa Lukuvi alifariki dunia Machi 25, 2026 wakati akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Benjamin Mkapa.








Na Mwandishi Wetu,Morogoro


MKUU wa Mkoa wa Morogoro, Adam Kighoma Malima, ameitaka Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA) pamoja na wakulima kuongeza uzalishaji wa mazao ya viungo kwa kuzingatia ubora, tija na ushindani wa soko la kimataifa, akisisitiza kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kufikia dira ya Taifa ya kukuza uchumi kupitia sekta ya kilimo.

Akizungumza katika mkutano wa wadau wa mazao ya viungo uliofanyika mkoani Morogoro, Malima amesema ni lazima wakulima washirikishwe kikamilifu katika kupanga na kutekeleza mikakati ya kilimo, huku akisisitiza umuhimu wa kuwepo kwa mifumo rafiki ya kifedha itakayowawezesha kumudu gharama za uzalishaji hasa kwa mazao yanayochukua muda mrefu kukomaa kama pilipili manga.

Amesema ili kuongeza ushindani wa mazao ya viungo katika soko la dunia, kuna haja ya kuimarisha vyama vya ushirika, kuboresha mbinu za kilimo na kuhakikisha wakulima wanapata elimu sahihi ya kilimo cha kibiashara pamoja na upatikanaji wa masoko ya uhakika.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa COPRA, Irene Mlola, amesema mamlaka hiyo imejipanga kuongeza uzalishaji wa mazao ya viungo kutoka tani 22,000 za sasa hadi kufikia tani 50,000 ifikapo mwaka 2030, sambamba na kuongeza ubora na thamani ya mazao hayo kupitia uchakataji.

Mlola amesema kwa sasa thamani ya mauzo ya nje ya mazao ya viungo imefikia takribani shilingi bilioni 497, huku akibainisha kuwa bado kuna fursa kubwa ya kupanua uzalishaji ili kunufaika zaidi na soko la dunia linalokadiriwa kufikia tani milioni 11 ambapo Tanzania inauza tani 1.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Batilda Burian, amesema ni wakati wa Tanzania kuacha kuuza mazao ghafi na badala yake kuongeza thamani kupitia uchakataji, akieleza kuwa mazao ya viungo yana fursa kubwa katika sekta za afya, lishe na vipodozi.

Amesema ukuaji wa soko la bidhaa za asili duniani, ikiwemo superfoods, unatoa nafasi kwa nchi kuongeza uzalishaji na kuimarisha ushindani, huku akihimiza uwekezaji zaidi katika teknolojia ya uchakataji ili kuongeza mapato na ajira.

Kwa upande wao, baadhi ya wakulima walioshiriki mkutano huo wamesema licha ya uwepo wa fursa nyingi katika kilimo cha mazao ya viungo, bado wanakabiliwa na changamoto za miundombinu duni ya barabara, ukosefu wa maghala ya kuhifadhi mazao pamoja na bei zisizo na ushindani kutokana na uwepo wa madalali wachache sokoni.

Wamesema kuna haja ya kuimarishwa kwa mafunzo ya kilimo cha kisasa, upatikanaji wa pembejeo bora na mifumo madhubuti ya masoko ili kuwawezesha kuongeza uzalishaji na kunufaika zaidi na sekta hiyo yenye mchango mkubwa katika uchumi wa Taifa.

COPRA imewakutanisha wadau ili kuweka juhudi za pamoja kuimarisha kilimo cha mazao ya viungo na kuongeza uzalishaji wenye tija unaolenga kufaidika na soko la ndani na lile la Kimataifa.








Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Muungano Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Bi. Cesilia Nkwamu akiwasilisha maelezo kuhusu andiko la ukumbi wa Karimjee kuwa Kituo cha Kumbukumbu na Nyaraka za Muungano (Makavazi) wakati wa kikao baina ya wataalamu kutoka Ofisi hiyo, Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa na Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kilichofanyika Machi 31, 2026 Jijini Dar es Salaam.

**************

Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) na Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam zimekubaliana kuandaa Hati ya Makubaliano (MoU) kwa ajili ya kuufanya Ukumbi wa Karimjee kuwa Sehemu ya Kituo cha Kutunza Kumbukumbu na Nyaraka za Muungano (Makavazi).

Akizungumza katika kikao baina ya wataalamu wa Ofisi hizo Machi 31, 2026 Jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Muungano Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Juma Mohammed Salum amesema makubaliano hayo ni utekelezaji wa maelekezo yaliyotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Dkt. Salum amesema Ofisi ya Makamu wa Rais ilipewa maelekezo mahsusi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kuanzisha Vituo Vya Kutunza Kumbukumbu na nyaraka Muungano (Makavazi) upande wa Tanzania Bara na Zanzibar ili kusaidia wananchi kuelewa chimbuko na misingi ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

“Makubaliano hayo yataweka msingi muhimu katika kutunza historia ya taifa letu kwani ukumbi wa karimjee ni moja ya eneo muhimu na sote kama tunavyokumbuka ndipo ambapo Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilizaliwa mwaka 1964” amesema Dkt. Salum.

Aidha Dkt. Salum amesema makubaliano hayo pia yatawezesha utunzaji na uhifadhi wa taarifa muhimu za Muungano ambazo ni muhimu kwa ajili ya mustakabali wa kizazi cha sasa na baadae na kuwa hatua hiyo inawezesha wananchi kufahamu manufaa ya Muungano.

“Zipo baadhi ya nchi duniani ikiwemo Ujerumani soko la historia ni muhimu sana kwa wanafunzi wa taifa hilo, hivyo sisi tumeona ni muhimu kutunza historia ya taifa letu kwa ajili ya vizazi vya sasa na vijavyo” amesema Dkt. Salum.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, Bw. Elihuruma Mabelya ameishukuru Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kuandaa andiko hilo na kuwa Ofisi yake itatoa ushirikiano unaohitajika ili kufanikisha wazo hilo ambalo ni muhimu kwa mustakabali wa taifa.

“Tunashukuru kwa wazo hili ambalo sisi kama Jiji tutahakikisha linapitia ngazi zote za maamuzi ikiwemo kujadiliwa na kupitishwa katika vikao vya Baraza la Madiwani ili kupata baraka na hatimaye kuanza utekelezaji” amesema Elihuruma.

Aidha Elihuruma alishauri kuundwa kwa kamati ndogo ya wataalamu kwa ajili ya kuratibu mpango kazi utakaondaliwa ambao utaongeza kasi ya utekelezaji wa malekezo yanayotolewa katika ngazi za maamuzi.

Kikao hicho cha siku moja kiliwashirikisha wataalamu kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam na Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa.

Mkurugenzi wa Muungano Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Juma Mohammed Salum akizungumza jambo wakati wa kikao baina ya wataalamu kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa na Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kilichofanyika Machi 31, 2026 Jijini Dar es Salaam ambacho kilijadili andiko la ukumbi wa Karimjee kuwa Kituo cha Kumbukumbu na Nyaraka za Muungano (Makavazi).
Baadhi ya wajumbe wa kikao kilichojadili kuhusu andiko la ukumbi wa Karimjee kuwa Kituo cha Kumbukumbu na Nyaraka za Muungano (Makavazi) kutoka Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam wakifuatilia majadiliano ya kikao hicho kilichofanyika Machi 31, 2026 Jijini Dar es Salaam ambacho kilijadili andiko la ukumbi wa Karimjee kuwa Kituo cha Kumbukumbu na Nyaraka za Muungano
Wajumbe wa kikao ya wataalamu kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa na Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam wakiwa katika kikao kilichojadili andiko la ukumbi wa Karimjee kuwa Kituo cha Kumbukumbu na Nyaraka za Muungano (Makavazi).
Mkurugenzi wa Kitengo cha Huduma za Sheria Ofisi ya Makamu wa Rais, Bw. Dustan Shimbo akizungumza jambo wakati wa kikao baina  ya wataalamu kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa na Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kilichofanyika Machi 31, 2026 Jijini Dar es Salaam ambacho andiko la ukumbi wa Karimjee kuwa Kituo cha Kumbukumbu na Nyaraka za Muungano (Makavazi).
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, Bw. Elihuruma Mabelya akizungumza jambo wakati wa kikao baina  ya wataalamu kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa na Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kilichofanyika Machi 31, 2026 Jijini Dar es Salaam ambacho kilijadili andiko la ukumbi wa Karimjee kuwa Kituo cha Kumbukumbu na Nyaraka za Muungano (Makavazi).
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Ofisi ya Makamu wa Rais, Bi. Sarah Kibonde akizungumza jambo wakati wa kikao baina  ya wataalamu kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa na Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kilichofanyika Machi 31, 2026 Jijini Dar es Salaam ambacho kilijadili andiko la ukumbi wa Karimjee kuwa Kituo cha Kumbukumbu na Nyaraka za Muungano (Makavazi).
Mkuu wa Kitengo cha Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) Ofisi ya Makamu wa Rais, Bi. Joyce Mnunguli akizungumza jambo wakati wa kikao baina  ya wataalamu kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa na Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kilichofanyika Machi 31, 2026 Jijini Dar es Salaam ambacho kilijadili andiko la ukumbi wa Karimjee kuwa Kituo cha Kumbukumbu na Nyaraka za Muungano (Makavazi)
Mkurugenzi wa Muungano Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Juma Mohammed Salum (kushoto mbele) akiwa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, Bw. Elihuruma Mabelya (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa kikao kilichojadili andiko la ukumbi wa Karimjee kuwa Kituo cha Kumbukumbu na Nyaraka za Muungano (Makavazi) kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam na Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa kilichofanyika Machi 31, 2026 Jijini Dar es Salaam.

Top News