Na Mwandishi Wetu


KATIKA hali isiyo ya kawaida, Mbunge wa Mkinga anayemaliza muda wake, Dastan Kitandula amekerwa kuuliza maswali chokonozi aliyodai yamepangwa na washindani wake kisiasa.

Kitandula ambaye pia ni Naibu Waziri Maliasili alionyesha kukerwa kwa kuuliza maswali hayo alipokuwa kwenye mkutano wa kampeni ya kuomba ridhaa ya wajumbe wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ili aweze kuteuliwa kutetea kiti chake.

Akiwa kwenye kata ya Daluni katika jimbo la Mkinga mkoani Tanga,  Kitandula aliulizwa maswali matatu yaliyomfanya ashindwe kuzuia hasira zake kutokana na aina ya maswali aliyokuwa akiulizwa wakati wa mkutano huo.

Swali la kwanza aliulizwa na mjumbe kutoka tawi la Kisiwani A ambapo aliuliza hivi; "Mheshimiwa mgombea, kanuni za uteuzi  katika vyombo vya dola katika fungu la kwanza la kanuni za jumla linalohusu mashariti ya uongozi, ibara ya 3 (I)…

“Linamtaka mbunge awe anatembelea jimbo lake mara kwa mara kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo ambayo imetengewa fedha na Serikali. Kwanini wewe huonekani mpaka uchaguzi ufike huku miradi ya zaidi ya sh bilion 3.9 fedha zilizoingizwa na Rais Samia Suluhu Hassan zikipotea,?". 

Wakati anajibu swali hilo, mgombea huyo alisema, "Nilijua tu lazima wewe uulize swali, Ningeshangaa kama usingeuliza swali, Najua mmetumwa kuuliza maswali haya,  kama pesa naleta na zinaliwa mimi kosa langu ni nini?.

Kana kwamba swali hilo halitoshi, mgombea huyo aliulizwa  swali la pili na kada mwingine wa CCM.

Kada huyo alihoji  kwanini vituo vingi vya afya kwenye maeneo mengine vimeingiziwa sh million 500 na vimeisha lakini kituo cha kata yetu ambacho awali kilikuwa zahanati haijaisha wakati tumeingiziwa pesa?.

Kitandula akajibu "Hapa kuna Mwenyekiti wa Kitongoji wa Kijiji na Diwani, wao wanafanya nini mpaka lawama mnipe mimi?.

Hata hivyo Mgombea huyo aliendelea kuandamwa na maswali alipofika kwenye kata ya Maramba ambapo kada mwingine wa CCM aliuliza hivi;

 "Mwaka 2023 mwishoni ulituambia mwaka uliopita 2024,  tutajengewe barabara ya lami ya urefu wa kilomita 10 , lakini Ilani ya uchaguzi ya mwaka 2025 hadi 2030 imeitaja barabara ya Maramba-Tanga kufanyiwa upembuzi yakinifu na sio kujengwa kwa kiwango cha lami

Je wewe uliposema kuna kilomita 10 na zingeisha mwaka jana, ulitudanganya?.

Swali hilo lilimfanya mgombea huyo apaniki ambapo alijibu akisema;

 "Achaneni na hao wanaosema kuhusu Ilani  nisikilizeni mimi, kilomita kumi zipo"

Akiwa katika kata ya Kigongo Magharibi, mgombea huyo anayeomba ridhaa kwa awamu nyingine ya tatu  aliulizwa hivi.

" Mh mgombea, kabla ya ubunge wako tulikuwa na mbunge Mwandoro aliyekaa kwa miaka 10 na katika awamu yake Barabara yetu hii ilikuwa inapitika muda wote, lakini wewe umekaa kwa miaka 15 na barabara ni mbovu inakera, je unazungumziaje kuhusu hilo.?

Swali hilo pia liimkera zaidi mgombea huyo  ambapo alijibu kwa kufoka akisema,

 "Msipende kutengenezewa maswali, hata mkipewa maswali yawekeni vizuri ili isionekane mmepewa maswali" 

Hata hivyo mgombea huyo aliendelea kusema kuwa "Barabara zetu za huku milimani hazina shukrani ndio maana kila mara zinaharibika, lakini tutaweka barabara za zege".

Jimbo hilo lina wagombea sita, lakini ushindani mkali upo kati ya Kitandula na Twaha Mwakioja pamoja na Saidi Duviii.


Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira) Profesa Peter Msofe ameonekana kuridhishwa na utendaji kazi na uwajibikaji wa watumishi wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) katika utekelezaji wa majukumu ya Mazingira hasa usimamizi wa utekelezaji wa Sheria ya Mazingira Nchini.

Hayo yamedhihirika wakati alipotembelea Ofisi za Baraza jijini Dar es Salaam kwa mara ya kwanza toka kuteuliwa kwake katika nafasi hiyo ya Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Mazingira.

Amesema "NEMC pamoja na changomoto zote, bado mmepiga hatua katika suala Zima la usimamizi wa utekelezaji wa Sheria ya Mazingira nchini.

Amesema "NEMC mnafanya kazi, watu wanaona na mnaonekana, licha ya changamoto mnazokumbana nazo, lakini endeleeni kufanya kazi kwa ajili ya manufaa ya Taifa la Tanzania, huku mkilinda Afya zenu dhidi ya Mazingira hatarishi katika Utekelezaji wa majukumu yenu" amesema Prof.Msofe.

Aidha ameainisha mambo matano ambayo watumishi wa NEMC wanatakiwa kuyazingatia katika utekelezaji wa majukumu ambayo ni kuweka uwiano kati ya vihatarishi binafsi na vihatarishi vya Mazingira ya kazi ili kuepuka madhara ya kiafya katika Utekelezaji wa majukumu, kujifunza na kushirikishana ujuzi wa utendaji kazi, ushirikiano mkubwa katika kazi na uvumbuzi katika maswala ya Mazingira ili kuweza kufanya kazi kwa kuendana na ulimwengu wa sasa.

Kwa upande wa Mkurugenzi Mkuu wa NEMC Dkt. Immaculate Sware Semesi alipozungumza ameesema bado NEMC inakabiliana na changamoto katika kutekeleza majukumu yake kutokana na kukosekana kwa Sheria inayotoa Mamlaka kamili ya Utekelezaji ambapo bado mchakato wa kuifanya NEMC kuwa Mamlaka unaendelea.











Mwenyekiti wa Kamisheni ya Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), Profesa John Kondolo, ameongoza ziara ya ukaguzi wa ujenzi wa jengo la Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (STU) la COSTECH jijini Dodoma, ambapo amepongeza hatua kubwa iliyofikiwa na mkandarasi anayejenga jengo hilo.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Julai 31, 2025 Jijini Dodoma Profesa Kondolo amesema kuwa wamejiridhisha na maendeleo ya ujenzi ambao umeendana na masharti ya mkataba unaotakiwa kukamilika ifikapo Machi 2026.

“Kiwango na ubora wa kazi tulivyoshuhudia vinatupa matumaini makubwa kwamba jengo hili jipya la STU litakuwa na hadhi ya kitaifa na kimataifa katika kuendeleza sekta za sayansi na teknolojia,” amesema Profesa Kondolo.

Ameeleza kuwa jengo hilo linajengwa kwa umadhubuti na heshima inayostahili taasisi muhimu ya COSTECH, hivyo linaonesha kukidhi viwango vya usanifu wa kisasa na matumizi ya muda mrefu.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH, Dkt. Amos Nungu, amesema kuwa mradi huo unatekelezwa kwa kutumia fedha za Serikali takriban shilingi bilioni nane za Kitanzania kupitia mradi wa HEET, ukiwa ni sehemu ya mikakati ya Serikali kuboresha miundombinu ya utafiti na ubunifu nchini.

Dkt. Nungu amefafanua kuwa jengo hilo litakuwa na kumbi za bunifu, kumbi za mikutano ya wanasayansi, na maabara za kisasa zitakazowezesha wabunifu kuwndeleza bunifu zao kwa ufanisi zaidi.

“Tunategemea pia kuwa na nafasi maalum kwa ajili ya wabunifu kupata huduma za Atamizi (incubation) ili kukuza mawazo na ubunifu mpya,baada ya makao makuu kuhamia Dodoma, nafasi iliyokuwa ikitumika Dar es Salaam itatumika kikamilifu kwa ajili ya huduma hizo,” ameeleza Dkt. Nungu.

Aidha, Dkt. Nungu amesema kuwa kukamilika kwa jengo hilo kutarahisisha uratibu wa shughuli za kitaifa za utafiti na teknolojia kutokana na uwepo wa miundombinu ya kisasa na mazingira bora ya kazi kwa wataalamu na wabunifu.

Kwa upande wake, Msanifu Majengo wa mradi huo, Benedict Martin, ameeleza kuwa usanifu wa jengo hilo umezingatia vigezo vya kisayansi na kiteknolojia kwa kuhakikisha linaendana na mahitaji ya utafiti na ubunifu wa kisasa.

Martin alisema usanifu huo umejumuisha ofisi za kisasa, kumbi za mafunzo, maeneo ya maonyesho ya teknolojia, na mifumo ya kidigitali itakayorahisisha mawasiliano ya kitaifa na kimataifa kwa COSTECH.

“Tumepanga kila kipengele kwa uangalifu mkubwa ili kuhakikisha kuwa linaweza kubeba shughuli zote za COSTECH kwa miongo kadhaa ijayo bila kuhitaji mabadiliko makubwa,” alisema Martin.

Kukamilika kwa jengo la STU kunatarajiwa kuimarisha zaidi nafasi ya Tanzania katika utafiti na maendeleo ya kisayansi, ikileta urahisi kwa wanasayansi, wabunifu na sekta binafsi kushirikiana katika kukuza teknolojia na ubunifu nchini.







Kampuni ya usafiri wa mtandaoni Bolt Tanzania kwa pamoja na Chama cha Madereva Mtandaoni Tanzania imezindua rasmi programu ya mafunzo ya siku 10 kwa madereva wake wa jiji la Dar es Salaam. Mafunzo hayo yalianza jana katika ghorofa ya tatu ya jengo la Tropical na yataendelea hadi Agosti 8.

Mpango huu unajumuisha vipengele vitatu muhimu: Mafunzo na vyeti vya Usafiri wa Umma (PSV) kwa kushirikiana na Taasisi ya Usafirishaji Tanzania (NIT); Moduli ya Bolt Best Practices inayolenga kukuza huduma bora na kujenga uaminifu kati ya dereva na mteja; na Mafunzo ya Misingi ya Kukabiliana na Dharura Barabarani, yatakayowawezesha madereva kushughulikia matukio kwa haraka na kwa usalama.

Huu ni mwendelezo wa dhamira ya Bolt kuhakikisha usalama, utiifu wa sheria, na uwezeshaji wa madereva nchini. Kupitia mafunzo haya, Bolt inalenga kuongeza taaluma ya madereva, kuwapa ujuzi wa kukabiliana na dharura, na kuwahamasisha kufuata sheria za Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA).

Utafiti wa hivi karibuni uliochapishwa na Tanzania Journal of Development Studies umebaini kuwa "ubora wa huduma, muda wa huduma, na mienendo ya kitaaluma ya madereva ndizo sababu kuu zinazowaridhisha wateja wa usafiri wa mtandaoni nchini Tanzania." Aidha, utafiti mwingine unaonyesha kuwa "asilimia zaidi ya 65 ya abiria huzingatia zaidi tabia ya madereva iliyo na heshima na weledi kama kigezo cha kuchagua jukwaa la usafiri mara kwa mara."

Dimmy Kanyankole, Meneja Mkuu wa Bolt Tanzania, amesema: “Matokeo haya yanaonesha umuhimu wa kuwekeza kwa kina katika taaluma ya madereva na uwezo wao wa kuwahudumia wateja kwa weledi – jambo ambalo Bolt na TODA wanalitekeleza moja kwa moja kupitia mpango huu.”

“Kupitia mafunzo haya ya darasani na kwa vitendo ya siku 10 kwa kushirikiana na TODA, madereva wanapata fursa ya kueleza changamoto zao na kujifunza mbinu bora za kushughulika na abiria wasumbufu pamoja na matukio yasiyotarajiwa barabarani,” aliongeza.









Na Karama Kenyunko, Michuzi Tv

MAMLAKA ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) na Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) wamesaini Mkataba wa Makubaliano (MoU) kwa lengo la kuimarisha ushirikiano kati ya sekta ya bima na masoko ya mitaji nchini.

Pia Taasisi hizo mbili zitashirikiana pamoja na ujumuishaji wa kifedha ili kuimarisha uwekezaji katika sekta ya bima.

Akizungumza katika hafla hiyo, Kamishna wa Bima Tanzania, Dkt Baghayo Saqware, ameeleza kuwa ushirikiano huo ni hatua muhimu katika kuhakikisha sekta ya bima inakuwa thabiti, shindani na jumuishi, sambamba na kuendana na mwelekeo wa Serikali ya Awamu ya Sita iliyochini ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa kukuza uchumi kupitia sekta binafsi.

"Ushirikiano huu utasaidia kuyafanya makampuni ya bima kuwa imara na stahimilivu, na hivyo wananchi kuendelea kupata kinga bora kwa mali, afya na uwekezaji wao, huku pia ukiboresha mifumo ya taarifa na kuwezesha kampuni hizo kuongeza mitaji kupitia soko la hisa,"amesema dkt Saqware

Amongeza kuwa makubaliano hayo ni fursa ya kuunganisha nguvu katika kukuza bidhaa bunifu za kifedha kama vile bima zinazoweza kuorodheshwa sokoni, pamoja na kutoa elimu kwa umma kuhusu masuala ya kifedha.

“TIRA inaamini mafanikio ya sekta ya bima hayawezi kutenganishwa na uimara wa masoko ya hisa ushirikiano huu unalenga kuimarisha mifumo ya taarifa, uwazi na uwajibikaji katika sekta hizi mbili muhimu,” amesema Sakware.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa DSE, Peter Nalitolela, amesisitiza kuwa makubaliano hayo ni dira ya kimkakati ya kuimarisha ujumuishaji wa kifedha kwa watanzania wote.

Amesema hatua hiyo inalenga kuboresha uwazi katika sekta za kifedha, kuongeza nidhamu ya fedha kwa taasisi, na kuchochea kasi ya mabadiliko ya kiuchumi, sambamba na kuhamasisha kampuni za bima kuwekeza kwenye soko la hisa ili kujenga uchumi imara na endelevu.

“Tutahamasisha kampuni za bima kutumia fursa ya soko la hisa kwa ajili ya kupata mtaji, kuimarisha utawala bora, na kukuza uelewa wa jamii juu ya uwekezaji,” amesema.

Makubaliano hayo yanajumuisha maeneo kadhaa ya ushirikiano ambayo ni kuandaa kampeni za elimu ya fedha kwa wananchi na wafanyabiashara wadogo, kuendesha mafunzo ya pamoja kwa kampuni za bima kuhusu mchakato wa kuorodheshwa DSE (IPO), na kuanzisha mikutano ya kila mwaka kati ya taasisi hizo mbili kwa lengo la kubadilishana uzoefu na taarifa.

Sekta ya masoko ya mitaji imeelezwa kuwa ina nafasi muhimu katika kusaidia kampuni za bima kupata mtaji wa muda mrefu, kuongeza uwazi wa kifedha na kuimarisha usimamizi wa hatari. Vilevile, makubaliano hayo yameainisha mpango wa pamoja wa kuandaa matukio kama siku ya Bima ya Kila Mwaka, ripoti za pamoja na mikutano ya wakurugenzi wa sekta husika.

Katika hotuba zao viongozi wa taasisi zote mbili walisisitiza kuwa makubaliano hayo si mwisho, bali mwanzo wa sura mpya ya ushirikiano wa kimkakati kwa maendeleo jumuishi na endelevu ya sekta ya fedha nchini Tanzania.

Viongozi hao wamesema makubaliano hayo ni hatua muhimu katika kufanikisha Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2050 na kujenga mfumo imara wa kifedha, huku wakihimiza wananchi na taasisi za bima kuendelea kutumia huduma za bima kwa kuwa sekta hiyo inasimamiwa ipasavyo.




Kamishna Bima Tanzania,  Baghayo Saqware (Kulia) na Afisa Mtendaji Mkuu wa Soko la Hisa Peter Nalitolela wakibadirishana nyaraka baada ya kusaini  mkataba wa makubaliano kati ya hizo sekta mbili. Hafla ya kutiliana saini kwa makubaliano hayo imefanyika leo Julai 31, 2025 jijini Dar es Salaam


WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dkt. Selamani Jafo, amesema kuwa ndani ya muda mfupi Tanzania haitahitaji tena kuagiza bidhaa muhimu kama mabati, vioo, nondo na saruji kutoka nje ya nchi, kutokana na ongezeko la uzalishaji wa bidhaa hizo nchini.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri Jafo tarehe 31 Julai 2025 wakati wa ziara ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan katika mkoa wa Pwani, ambapo alizindua rasmi Kongani ya Viwanda ya Kwala pamoja na Bandari Kavu ya Kwala.

“Kwa mfano, mahitaji ya mabati kwa mwaka ni tani 130,000. Leo hii, makampuni yote yanayozalisha mabati hapa nchini, ikiwemo Lodhia, King Lion, Alaf na mengineyo, yamefikia uzalishaji wa tani 260,000 kwa mwaka. Hii ina maana tunakuwa na ziada ya tani 130,000,” alisema Waziri Jafo.

Aliongeza kuwa hatua hii ni sehemu ya mpango mpana wa Serikali kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara kuhakikisha kuwa Tanzania inajenga uchumi wa viwanda unaojitosheleza kwa bidhaa za msingi, huku pia ikiongeza uwezo wa kusafirisha bidhaa nje ya nchi na kuingiza fedha za kigeni.

Kwa mujibu wa Waziri Jafo, Eneo la Kwala lina zaidi ya hekta 1,000, ambapo zaidi ya viwanda 200 vinatarajiwa kujengwa kwa uwekezaji unaozidi dola za Kimarekani bilioni 3. Inakadiriwa kuwa bidhaa zitakazozalishwa kwenye kongani hiyo zitaweza kuingiza jumla ya dola bilioni 6 kwa mwaka, ambapo dola bilioni 4 zitabaki kwa matumizi ya ndani, na dola bilioni 2 zitatokana na usafirishaji wa bidhaa nje ya nchi.

Waziri Jafo alisisitiza kuwa Wizara itaendelea kusimamia maono ya Rais Samia ya kuifanya Tanzania kuwa kinara wa uzalishaji wa bidhaa Afrika Mashariki, na sehemu nyingine duniani.
Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Samwel M. Maneno amefanya mazungumzo na Ujumbe kutoka Kampuni ya Kimataifa ya Mawakili ya Curtis ( Curtis, Mallet-Prevost,Colt&Mosle LLP Law firm) kwa nia ya kuanzisha fursa za ushirikiano katika maeneo mbalimbali kati ya Kampuni hiyo na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Naibu Mwanasheria Mkuu amezungumza na ujumbe huo tarehe 30 Julai, 2025 kwa njia ya mtandao, ambapo alianza kwa kuwashukuru Kampuni ya Mawakili ya Curtis kwa utayari wao wa kushirikiana na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali katika kuwajengea uwezo Mawakili wa Serikali katika maeneo mbalimbali ya Sheria.

Akizungumza wakati wa kikao hicho, Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali alieleza kuwa kwa sasa Tanzania imekuwa ikitekeleza miradi mikubwa katika Sekta mbalimbali ikijumuisha Sekta ya Miundombinu, Uchukuzi, Nishati, Madini, Mawasiliano, Biashara na Uwekezaji.

Aidha, akizungunzia eneo la Uwekezaji, Mhe. Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali ameelezea dhamira ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya Uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kufungua fursa za Uwekezaji, hatua ambayo imeiwezesha Tanzania kuwa kituo bora cha Uwekezaji barani Afrika.

"Nchi yetu kwa sasa inafunguka zaidi katika eneo la Uwekezaji, na hii inatokana na maboresho makubwa ya kisera , mazingira wezeshi ya Biashara na Ushirikiano mkubwa na sekta binafsi hususan katika sekta za kibiashara, nishati, miundombinu yanayoendelea kufanywa na Serikali ya Awamu ya Sita, hivyo ninapenda kuwakaribisha kushirikiana nasi.'. Amesema Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali

Aidha, Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali alisisitiza kuwa kutokana na uwekezaji mkubwa unaofanywa na nchi yetu katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati, kuna umuhimu mkubwa kwa Mawakili wa Serikali kujengewa uwezo wa kitaaluma wa kimataifa katika nyanja mbalimbali ikiwa ni pamoja na majadiliano, usimamizi wa mikataba, utatuzi wa migogoro na kushikishwa katika Kampuni kubwa za uwakili duniani.

Akizungunza kwa niaba ya Kampuni ya Mawakili ya Curtis, Bi. Lise Johnson aliipongeza Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kuona umuhimu wa kuongeza ujuzi kwa Mawakili wa Serikali na kuahidi ushirikiano katika eneo hilo kulingana na uzoefu mkubwa walionao katika nyanja mbalimbali za Sheria.

Aidha, amezungumzia uzoefu walionao katika nyanja mbalimbali za Sheria ikiwa ni pamoja na maeneo ya Ushindani, uendeshaji wa mashauri, usuluhishi wa migogoro, uwekezaji na biashara, ulinzi wa taarifa, faragha na mtandao, Fedha, Hakimiliki, Dhamana na Mtaji, Kodi, majadiliano ya Mikataba, Mikataba ya Ujenzi, Nishati, Mafuta na Gesi, na Maktaba Mtandao( e- library) .

Kampuni ya Curtis Law Firm ni Kampuni ya Kimataifa yenye Ofisi zake nchini Marekani, Amerika ya Kusini, Ulaya, na Mashariki ya Kati ikiwa na uzoefu wa muda mrefu katika maeneo ya Sheria na imekuwa ikishirikiana na nchi zinazoendelea kutoa msaada katika maeneo mbalimbali ikiwepo uendeshaji wa mashauri kwenye Mahakama za kimataifa pamoja na Mabaraza ya Usuluhishi ya Kimataifa ( International Arbitration Tribunals).

Miongoni mwa nchi zinazoendelea ambazo Kampuni hiyo imefanya kazi nazo ni Uganda, Nigeria, Cameroon, Panama, Colombia na Argentina.

Kikao hicho kilichoongozwa na Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, kilihudhuriwa pia na Mkurugenzi wa Mikataba na Makubaliano Bi. Sia Mrema, Wakili wa Serikali Mkuu Bi. Felista Lelo, Wakili wa Serikali Mkuu Bi. Catherine Paul na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Bi. Leila Muhaji.

Mradi wa Kuimarisha na Kuboresha Elimu ya Awali na Msingi (BOOST) imewezesha vifaa vya TEHAMA katika shule teule na vituo vya walimu 400 ili kurahisisha ujifunzaji na ufundishaji kwa njia za kisasa.

Aidha imewajengea uwezo walimu 600 wa TEHAMA, walimu wakuu 600, na waratibu elimu kata 450 namna ya kutumia vifaa hivyo kwa tija katika mazingira ya kufundishia.

Mwalimu wa TEHAMA katika Shule ya Msingi Ramadhani iliyopo katika Halmashauri ya Mji wa Njombe Silivia Mbilinyi, amesema kuwa mafunzo hayo yamekuwa chachu ya mabadiliko katika mbinu za kufundishia, na sasa wanafunzi wanashiriki kikamilifu darasani kupitia matumizi ya vifaa vya TEHAMA.

Naye, mwalimu Erasto William katika Shule ya Msingi Nyambogo iliyopo katika Halmashauri ya Makambako amesema kuwa walimu wengi wameweza kubuni mbinu bunifu za kufundisha, na hivyo kuifanya elimu kuwa ya kuvutia na ya kisasa zaidi kwa wanafunzi wa shule za msingi.









Songea_Ruvuma.

Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Mkoa wa Ruvuma limetangaza katizo la umeme litakalotokea katika Wilaya ya Songea siku ya Jumamosi, tarehe 2 Agosti 2025, kuanzia saa 3:00 asubuhi hadi saa 10:00 jioni.

Taarifa hiyo imetolewa na Afisa Uhusiano na Huduma kwa Wateja wa shirika hilo, Alan Njiro, ambaye amesema kuwa katizo hilo ni sehemu ya maboresho ya huduma za umeme katika mji wa Songea.

Kwa mujibu wa Njiro, kazi zitakazofanyika ni pamoja na kubadilisha nguzo za miti ambazo zimekuwa mbovu na kuweka nguzo za zege zenye uimara zaidi, ambapo miti inayoathiri usalama wa nyaya za umeme itakatwa ili kuhakikisha usambazaji wa umeme unafanyika kwa ufanisi na bila hatari kwa wananchi.

Ameyataja maeneo yatakayoathirika na katizo hilo ni pamoja na Soko Kuu la Songea, Hospitali ya Mkoa, Mahakama Kuu, Ofisi za Mkuu wa Mkoa na Wilaya, Magereza, Songea Girls, RMA, pamoja na maeneo ya makazi kama Ruvuma Juu, Kipera, Liwena, Mateka, Ndilimalitembo, Matogoro Minarani, Mahenge, Makambi, Chandamali, Unangwa, Seedfarm, Matogoro, Chemchem na Boys.

Amesema TANESCO inawaomba radhi wateja wake kwa usumbufu utakaojitokeza wakati wa utekelezaji wa kazi hizo muhimu, Shirika hilo pia limetoa shukrani kwa wateja wake kwa uvumilivu wao, likisisitiza kuwa maboresho haya ni sehemu ya juhudi za kuboresha huduma ya umeme katika Mkoa wa Ruvuma.


Na Philomena Mbirika, Karatu Arusha.

Mamlaka ya hifadhi ya eneo la Ngorongoro (NCAA) imehitimisha maadhimisho ya siku ya askari Wanyamapori duniani kwa kufanya michezo mbalimbali iliyohususu askari wa Jeshi la Uhifadhi, askari wa Jeshi la polisi wilaya ya Karatu pamoja na kufanya shughuli ya upandaji miti katika shule ya Sekondari Welwel iliyopo Karatu Mkoani Arusha.

Kamishna wa Uhifadhi NCAA ameongoza maafisa na askari katika zoezi la kupanda miti Shule ya Sekondari Welweli, kutoa elimu ya shughuli za uhifadhi na utunzaji wa mazingira kwa wanananchi na kuongoza watumishi hao katika michezo mbalimbali ikiwemo kukimbia kilomita tano, mchezo wa mpira wa miguu kati ya askari wa jeshi la Uhifadhi kutoka pori lla akiba Pololeti, askari walioko eneo la hifadhi ya Ngorongoro pamoja na Polisi Karatu.

“NCAA ni sehemu ya Jamii, katika utekelezaji wa majukumu yetu tunashirikiana na vyombo vingine ikiwepo Polisi Wilaya za Ngorongoro na karatu pamoja na wananchi, ndio maana leo tumefanya michezo ya riadha, mazoezi yaa viungo, mchezo wa mpira wa miguu ili kuendelea kutuweka pamoja hasa katika shughuli za kuimarisha usalama na ulinzi wa rasilimali za Nchi) alifafanua Kamaishna Badru.

Badru ameeleza kuwa NCAA pia ina jukumu la kutoa elimu ya mazingira na uhifadhi shirikishi kwa jamii zinazozunguka hifadhi ya Ngorongoro, hivyo katika kuadhimisha siku ya askari wa Wanyamapori imetoaa miti bure kwa wananchi ili wakapande katika maeneo yao na kupanda miti katika shule ya Sekondari Welwel kisha kuzungumza na walimu na wanafunzi wa shule hiyo na kuwasisitiza kutunza miti iliyopandwa pamoja na mazingira kwa ujumla.

Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Karatu, Katibu tawala wa Wilaya hiyo Bw. Bahati Mfungo ameipongeza NCAA kwa ushirikiano inaotoa kwa wananchi wa Wilaya ya Karatu hasa kuwapa elimu ya mazingira, upandaji miti, kupambana na mgongano kati ya Wanyamapori na wananchi pamoja na kusaidia miradi mbalimbali ya wananchi ikiwemo huduma za kijamii.

Siku ya Askari wa Wanyamapori Duniani ilianza kuadhimishwa mwaka 2007 kwa lengo la kuwakumbuka askari waliopoteza maisha wakati wa kutekeleza majukumu yao, kauli mbiu ya maashimisho ya mwaka huu ni “ Rangers: Powering Transformative Conservation” ikilenga kuutambua mchango wa askari wa Wanyamapori katika kuleta mabadiliko ya kweli katika uhifadhi wa maliasili ambayo ni urithi wa Taifa.






Na Mwamvua Mwinyi, Pwani

Waziri wa Viwanda na Biashara, Dkt. Selamani Jafo ameeleza kuwa ,ndani ya muda mfupi, Tanzania haitakuwa na haja ya kuagiza bidhaa mbalimbali za ujenzi kutoka nje ya nchi kama mabati, vioo, nondo, na saruji. 

Haya yamebainika Julai 31 ,2025 wakati wa ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, mkoani Pwani, ambako alizindua Kongani ya Viwanda Kwala pamoja na Bandari Kavu . 

“Kwa mfano, mahitaji ya mabati kwa mwaka ni tani 130,000, lakini kwa sasa uzalishaji wa ndani umefikia tani 260,000 kupitia makampuni kama Lodhia, King Lion, ALAF na mengineyo. 

"Hii ina maana tuna ziada ya tani 130,000 , hivyo hakuna tena haja ya kuagiza kutoka nje,” alisema Waziri Jafo.

Aliongeza kuwa lengo kuu la serikali ni kupunguza kwa kiwango kikubwa uingizaji wa bidhaa kutoka nje na badala yake kuongeza uzalishaji wa ndani na kusafirisha bidhaa nje ya nchi, hatua itakayosaidia taifa kuingiza fedha za kigeni.

Kwa mujibu wa Dkt. Jafo, kongani ya viwanda Kwala ina jumla ya zaidi ya hekta 1,000 na inatarajiwa kuwa na viwanda zaidi ya 200, huku uwekezaji wake ukikadiriwa kuwa zaidi ya dola bilioni 3 za Kimarekani. 

Inatarajiwa kwamba bidhaa zitakazozalishwa kwa mwaka zitakuwa na thamani ya hadi dola bilioni 6, ambapo bilioni 2 zitatokana na mauzo ya nje na bilioni 4 kwa matumizi ya ndani.

“Wizara yangu itasimamia kwa karibu maono ya Mhe. Rais Samia ya kuifanya Tanzania kuwa nchi ya mfano katika sekta ya viwanda , tukizalisha zaidi kwa ajili ya soko la ndani na la nje,” alisisitiza.


Kassim Nyaki, NCAA.


Kamishna wa Mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro Abdul-razaq Badru amewataka askari wa uhifadhi wa taasisi hiyo kuendelea kulinda rasilimali za wanyamapori, Misitu na malikale kwa ari na weledi ili taifa liendelee kunufaika na rasilimali hizo.

Kamishna Badru ametoa maelekezo hiyo katika kilele cha siku ya askari wanyamapori duniani (World Rangers Day) leo tarehe 31 Julai, 2025 ambapo mamlaka hiyo imedhimisha siku hiyo katika viwanja vya mnadani Karatu Mkoani Arusha.

Amesema mamlaka inatambua mchango wa askari wa uhifadhi kutokana na kujitoa kwao kulinda rasilimali hizo hivyo iko tayari kuboresha utendaji wao ili uendane na mabadiliko ya sayansi na teknolojia. Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kwa kutambua mchango huo imewapa vyeti na fedha kufuatia juhudi na kujitoa kwao katika ulinzi wa kupambana na vitendo vya ujangili hali iliyosaidia kuokoa rasilimali za wanyamapori, mali za shirika na askari wengine.

“Maadhimisho haya ni maalum kwa ajili ya kutambua na kuenzi mchango wa askari wanyamapori wanaolinda hifadhi na rasilimali zilizopo, Tanzania ikiwa miongoni mwa mataifa yenye urithi mkubwa wa bioanuai, inao wajibu wa kuwaenzi askari wa uhifadhi ambao ni mashujaa wetu wa ulinzi wa wanyamapori na misitu kwa maslahi ya nchi yetu na vizazi vijavyo”alisema Kamishna Badru.

Akielezea maadhimisho ya siku hiyo Kaimu Meneja Idara ya Huduma za Ulinzi Mhifadhi Mwandamizi Linus Tiotem ameeleza kuwa tangu kuanzishwa kwa Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro jumla ya askari 11 wamepoteza maisha kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo ujangili, ujambazi na kuuawa na wanyamaopri.

Siku ya Askari wa Wanyamapori Duniani ilianza kuadhimishwa mwaka 2007 kwa lengo la kuwakumbuka askari waliopoteza maisha wakati wa kutekeleza majukumu yao, kauli mbiu ya maashimisho ya mwaka huu ni “ Rangers: Powering Transformative Conservation” ikilenga kuutambua mchango wa askari wa Wanyamapori katika kuleta mabadiliko ya kweli katika uhifadhi wa maliasili ambayo ni urithi wa Taifa.













Top News