Na Mwandishi Wetu
KATIKA hali isiyo ya kawaida, Mbunge wa Mkinga anayemaliza muda wake, Dastan Kitandula amekerwa kuuliza maswali chokonozi aliyodai yamepangwa na washindani wake kisiasa.

Akiwa kwenye kata ya Daluni katika jimbo la Mkinga mkoani Tanga, Kitandula aliulizwa maswali matatu yaliyomfanya ashindwe kuzuia hasira zake kutokana na aina ya maswali aliyokuwa akiulizwa wakati wa mkutano huo.
Swali la kwanza aliulizwa na mjumbe kutoka tawi la Kisiwani A ambapo aliuliza hivi; "Mheshimiwa mgombea, kanuni za uteuzi katika vyombo vya dola katika fungu la kwanza la kanuni za jumla linalohusu mashariti ya uongozi, ibara ya 3 (I)…
“Linamtaka mbunge awe anatembelea jimbo lake mara kwa mara kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo ambayo imetengewa fedha na Serikali. Kwanini wewe huonekani mpaka uchaguzi ufike huku miradi ya zaidi ya sh bilion 3.9 fedha zilizoingizwa na Rais Samia Suluhu Hassan zikipotea,?".
Wakati anajibu swali hilo, mgombea huyo alisema, "Nilijua tu lazima wewe uulize swali, Ningeshangaa kama usingeuliza swali, Najua mmetumwa kuuliza maswali haya, kama pesa naleta na zinaliwa mimi kosa langu ni nini?.
Kana kwamba swali hilo halitoshi, mgombea huyo aliulizwa swali la pili na kada mwingine wa CCM.
Kada huyo alihoji kwanini vituo vingi vya afya kwenye maeneo mengine vimeingiziwa sh million 500 na vimeisha lakini kituo cha kata yetu ambacho awali kilikuwa zahanati haijaisha wakati tumeingiziwa pesa?.
Kitandula akajibu "Hapa kuna Mwenyekiti wa Kitongoji wa Kijiji na Diwani, wao wanafanya nini mpaka lawama mnipe mimi?.
Hata hivyo Mgombea huyo aliendelea kuandamwa na maswali alipofika kwenye kata ya Maramba ambapo kada mwingine wa CCM aliuliza hivi;
"Mwaka 2023 mwishoni ulituambia mwaka uliopita 2024, tutajengewe barabara ya lami ya urefu wa kilomita 10 , lakini Ilani ya uchaguzi ya mwaka 2025 hadi 2030 imeitaja barabara ya Maramba-Tanga kufanyiwa upembuzi yakinifu na sio kujengwa kwa kiwango cha lami
Je wewe uliposema kuna kilomita 10 na zingeisha mwaka jana, ulitudanganya?.
Swali hilo lilimfanya mgombea huyo apaniki ambapo alijibu akisema;
"Achaneni na hao wanaosema kuhusu Ilani nisikilizeni mimi, kilomita kumi zipo"
Akiwa katika kata ya Kigongo Magharibi, mgombea huyo anayeomba ridhaa kwa awamu nyingine ya tatu aliulizwa hivi.
" Mh mgombea, kabla ya ubunge wako tulikuwa na mbunge Mwandoro aliyekaa kwa miaka 10 na katika awamu yake Barabara yetu hii ilikuwa inapitika muda wote, lakini wewe umekaa kwa miaka 15 na barabara ni mbovu inakera, je unazungumziaje kuhusu hilo.?
Swali hilo pia liimkera zaidi mgombea huyo ambapo alijibu kwa kufoka akisema,
"Msipende kutengenezewa maswali, hata mkipewa maswali yawekeni vizuri ili isionekane mmepewa maswali"
Hata hivyo mgombea huyo aliendelea kusema kuwa "Barabara zetu za huku milimani hazina shukrani ndio maana kila mara zinaharibika, lakini tutaweka barabara za zege".
Jimbo hilo lina wagombea sita, lakini ushindani mkali upo kati ya Kitandula na Twaha Mwakioja pamoja na Saidi Duviii.