Na Stella Kalinga, Simiyu
Mkoa wa Simiyu umejipanga kuhakikisha hakuna maambukizi mapya ya VVU ifikapo mwaka 2020, kwa kuwaanzishia dawa za kufubaza VVU wote watakaopimwa na kubainika kuwa na VVU bila kujali wingi wa CD4 kama mwongozo mpya unavyoeleza.

Hayo yamesemwa na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Dkt. Mageda Kihulya  wakati akitoa taarifa ya hali ya maambukizi ya VVU na Ukimwi katika Uzinduzi wa Kampeni ya Huduma Jumuishi za kuzuia maambukizi ya VVU  uliofanyika kimkoa katika viwanja vya Sabasaba Mjini Bariadi.  
Dkt Mageda amesema hadi kufikia Septemba 2016 Mkoa umesajili wateja 40,426 kwenye huduma za tiba na matunzo (CTC) na kati ya hao 34,838 tayari walikuwa wameanzishiwa  dawa za ARV sawa na asilimia 86,huku wagonjwa wanaoendelea na dawa za kufubaza VVU ni 18,246 sawa na asilimia 52.
Katibu Tawala mkoa wa Simiyu, Jumanne Sagini (wa pili kulia) akikata utepe katika Uzinduzi wa Kampeni ya Huduma Jumuishi za Kuzuia Maambukizi ya Virusi vya Ukimwi Kimkoa, uliofanyika katika uwanja wa Sabasaba Mjini Bariadi, (wa tatu kulia) Meneja wa AMREF Tanzania, Dkt.Amosi Nyirenda.

Dkt. Mageda ameongeza kuwa katika kipindi cha Januari hadi Desemba 2015 wananchi wapatao 262,862 walipata huduma ya ushauri nasaha na upimaji na kati yao 8,631 walibainika kuwa na maambukizi ya VVU sawa na asilimia 3.3 chini ya kiwango cha maambukizi cha kitaifa ambacho ni asilimia 5.1.

Aidha, akina mama wajawazito wapatao 92,964 katika kipindi cha Januari- Desemba 2015, waliohudhuria kliniki walipimwa kujua hali ya afya zao ikiwa ni kutekeleza mpango kabambe wa kuzuia maambukizi yaVVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto kati yao akinamama 1,459 waligundulika  kuwa na virusi sawa na 1.6%.

Sanjari na hilo Mganga Mkuu huyo wa Mkoa ameanisha mikakati ya kuzuia maambukizi mapya ya VVU  ifikapo 2020 Mkoani Simiyu, kuwa ni pamoja na kutoa  huduma za ushauri nasaha na upimaji kuwawezesha watu  kujua  hali zao na kujikinga na kukinga wenzao wasipate maambukizi  mapya, sambamba na kuwaanzishia dawa za kufubaza virusi wale wote watakaopimwa na kubainika na VVU bila kujali wingi wa CD4 kama mwongozo mpya  unavyoeleza.
Katibu Tawala mkoa wa Simiyu, Jumanne Sagini akipokea taarifa kutoka kwa Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya cha Muungano Mjini Bariadi, alipotembelea kituo hicho kujionea utoaji wa huduma za afya kabla ya Uzinduzi wa Kampeni ya Huduma Jumuishi za Kuzuia Maambukizi ya Virusi vya Ukimwi Kimkoa, uliofanyika katika uwanja wa Sabasaba.

Mikakati mingine ni  na kupima na kuanzisha  dawa za kufubaza VVU kwa akinamama wote wajawazito na wanao nyonyesha watakaobanika  na VVU, kutoa huduma ya tohara ya hiari  kwa wanaume na kuwafanyia uchunguzi wa Kifua Kikuu na kuwatibu mara kwa mara watakaobainika  kuwa na Kifua Kikuu kwani ni moja ya magonjwa nyemelezi yanayoua watu wengi.

Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka, Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Jumanne Sagini, amesema kuwa Kampeni ya Huduma Jumuishi za kuzuia Maambukizi ya VVU  itatekelezwa hadi Juni 2017, ambapo inalenga kufikia watu zaidi ya 6,000 katika wilaya zote za mkoa huu, huku akitoa rai kwa wadau kufuata sera, miongozo na sheria za Nchi katika kutoa huduma za VVU na Ukimwi wakati na baada ya kampeni hii.

Kwa upande wake Meneja wa AMREF Tanzania Dkt. Amosi  Nyirenda amesema Shirika hilo linafanya kazi kwa kushirikiana na Serikali katika mapambano dhidi ya UKIMWI na amewaomba wakazi wa Mkoa wa Simiyu kujenga utamaduni  wa kupima ili kujua afya zao wanapobaini wameathirika ni vema kuanza dawa mapema. 

“Sisi kama AMREF tunafanya kazi na Serikali kuhakikisha tunashirikiana  katika mapambano maeneo yote,   tunakwenda zaidi maeneo yenye uhitaji leo tumezindua kampeni hii hapa na tutaendelea na  kata  25 mpaka Desemba mwaka huu na mwaka ujao tutaenda kata 18 za mkoa wa Simiyu tutashirikiana na timu ya mkoa kuanisha kata husika” alisema Dkt.Nyirenda.

Uzinduzi wa Kampeni ya Huduma Jumuishi za kuzuia Maambukizi ya VVU Mkoa wa Simiyu, umeenda sambamba na uchangiaji wa damu kwa hiari, huduma za upimaji VVU, Toharakinga kwa wanaume, huduma za kuzuia maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto, huduma za magonjwa ya ngono na via vya uzazi, upimaji wa saratani ya shingo ya kizazi na huduma za ushauri wa lishe bora.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...