Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo ya Mitaji (UNCDF), kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Nishati, kwa msaada wa Umoja wa Ulaya (EU), wameandaa Kongamano la Kitaifa la Nishati Safi ya Kupikia la siku mbili lililoanza jijini Arusha jana, likiwakutanisha wadau wakuu wa nishati safi ya kupikia, wizara na taasisi za serikali, sekta binafsi, wafadhili, washirika wa maendeleo, asasi za kiraia, na watafiti, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano na kuharakisha mabadiliko kitaifa kuelekea katika matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Kongamano hilo la siku mbili lililozinduliwa rasmi na Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, ambapo wadau walijadili fursa na mikakati ya kuharakisha matumizi ya nishati safi ya kupikia ili kufikia lengo la asilimia 80 ya kaya kutumia nishati hiyo ifikapo mwaka 2034.

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Umoja wa Ulaya, UNCDF na wadau mbalimbali inaendelea kuimarisha jitihada za kuongeza upatikanaji wa nishati safi ya kupikia kupitia maboresho ya sera na mifumo ya udhibiti, kutafuta rasilimali fedha, kutoa elimu kwa jamii na kuimarisha ushiriki wa sekta binafsi.

Licha ya mafanikio yaliyopatikana, matumizi ya kuni na mkaa bado ndiyo chanzo kikuu cha nishati ya kupikia kwa kaya nyingi nchini. Kuongeza matumizi ya nishati safi ni muhimu katika kuboresha afya za wananchi, kulinda mazingira na kuwawezesha wanawake na vijana ambao huathirika zaidi na athari za matumizi ya nishati za asili.

Chini ya kaulimbiu "Kuendeleza Mustakabali wa Nishati Safi ya Kupikia Tanzania: Mafanikio, Ushirikiano na Njia za Kufikia Asilimia 80 ya Matumizi ifikapo 2034," mkutano huo ulionesha mafanikio yaliyofikiwa, kubaini changamoto zilizopo na kuweka mikakati mipya ya kuongeza matumizi ya nishati safi nchini. Wadau walisisitiza umuhimu wa uratibu na ushirikiano katika utekelezaji, pamoja na kuwepo kwa mifumo madhubuti ya ufuatiliaji na uwajibikaji ili kuhakikisha uwazi na matokeo yanayopimika.

Akizungumza katika mkutano huo, Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, alisisitiza dhamira ya Serikali akisema Serikali ya Tanzania imejipanga kikamilifu kuhakikisha inafikia lengo la asilimia 80 ya matumizi ya nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.

“Mkutano huu umetuwezesha kuoanisha sera, mifumo ya ufadhili na mikakati ya ushirikishwaji wa jamii ili kuharakisha utekelezaji, nishati safi ya kupikia ni muhimu katika kulinda afya za wananchi, kuwawezesha wanawake na vijana, pamoja na kuhifadhi mazingira yetu," alisema.

Aidha, alieleza kuwa juhudi za Mheshimiwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan katika kuhamasisha matumizi ya nishati safi zimekuwa chachu ya mabadiliko, huku kampeni za kitaifa zinazosimamiwa na UNCDF zikisaidia kuongeza uelewa wa wananchi na kubadili mitazamo kuhusu matumizi ya teknolojia za kisasa za kupikia.

Naye Balozi wa Umoja wa Ulaya nchini Tanzania na Jumuiya ya Afrika Mashariki, Bi. Christine Grau, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano, akibainisha kuwa, Umoja wa Ulaya umetenga euro milioni 30, sawa na zaidi ya shilingi bilioni 92 za Kitanzania, kwa ajili ya kupanua upatikanaji wa nishati safi ya kupikia, kuimarisha masoko ya nishati endelevu, kulinda rasilimali asili na kuzalisha fursa za kiuchumi.

“Huu ndio ufadhili mkubwa zaidi wa Umoja wa Ulaya katika sekta ya nishati safi ya kupikia katika nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara, ukiendana na mkakati wa Global Gateway unaolenga kuchochea uwekezaji wa sekta binafsi, kuhimiza ubunifu na kuleta matokeo yenye tija”, akiongeza kuwa msaada huo ni sehemu ya mkakati mpana wa kikanda wa kukuza maendeleo ya sekta binafsi na kupanua matumizi ya nishati safi ya kupikia barani Afrika.

Mkutano huo umefanyika wakati Tanzania ikiendelea kushuhudia mafanikio katika utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia (2024–2034). Kwa mujibu wa ripoti ya mkakati huo, matumizi ya nishati safi ya kupikia yameongezeka kutoka asilimia 16 mwaka 2022 hadi asilimia 28.6 kufikia Machi 2026. Mafanikio hayo yamechangiwa na ruzuku ya mitungi ya gesi ya LPG, kupunguzwa kwa gharama za umeme, kuondolewa kwa baadhi ya kodi kwenye vifaa vya nishati safi ya kupikia pamoja na uwekezaji wa sekta binafsi na washirika wa maendeleo.

Kwa mujibu wa Shirika la Kimataifa la Nishati (IEA), zaidi ya watu bilioni 2.3 duniani bado hawana huduma za nishati safi ya kupikia, huku Bara la Afrika likiwa na idadi kubwa zaidi. Hivyo, juhudi za Tanzania zinachangia si tu katika kufikia malengo ya maendeleo ya taifa, bali pia katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, kuboresha afya za jamii na kuimarisha usawa wa kijinsia duniani.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mshauri Mkuu wa Masuala ya Ufundi wa UNCDF, Bw. Peter Malika alisema, UNCDF ina jukumu la kuwezesha upatikanaji wa mitaji kwa ajili ya maendeleo ya jamii kwa kuondoa vikwazo vinavyokwamisha uwezo wa wananchi kumudu gharama, usambazaji wa bidhaa na upatikanaji wa mitaji kwa biashara.

“Kupitia programu ya CookFund, tunawezesha upatikanaji wa fedha, kujenga ushirikiano na kusaidia biashara na wabunifu kuhakikisha suluhisho za nishati safi ya kupikia zinawafikia Watanzania wote."

“Kupitia programu hii UNCDF imeendelea kutoa mitaji kwa biashara ndogo na za kati ili kusaidia upanuzi wa teknolojia za nishati safi ya kupikia, kuchochea ubunifu na kuongeza ajira”, aliongeza Bw. Malika.

Tangu kuanzishwa kwake, programu hiyo imetoa zaidi ya dola za Marekani milioni 11.2 kupitia ruzuku 102 kwa biashara ndogo na za kati, na kusaidia ajira takribani 27,000 nchini.

Programu hiyo imewezesha zaidi ya kaya 413,000 kupata huduma za nishati safi ya kupikia, zikiwanufaisha karibu watu milioni 1.94 nchini kote. Aidha, imeziwezesha biashara 961 na taasisi za umma 45, ikiwemo shule zinazotumia briketi, majiko ya umeme ya shinikizo (EPC), gesi ya LPG na nishati nyingine endelevu. Hatua hizi zimechangia kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa huku zikiboresha ufanisi, usalama na ubora wa huduma za upishi katika taasisi.

Katika sekta ya elimu pekee, wanafunzi 62,105 kutoka wilaya 14 katika mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Morogoro, Dodoma na Mwanza wamenufaika na programu hiyo, hatua iliyobooresha mazingira ya kujifunzia na kupunguza madhara yatokanayo na moshi. Kwa ujumla, utekelezaji wa CookFund umechangia kupunguza zaidi ya tani milioni 3.8 za hewa ukaa (CO₂e), na hivyo kusaidia Tanzania kufikia malengo yake ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na kuonesha nguvu ya ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi.

Mkutano huo umehitimishwa kwa Serikali, wafadhili na sekta binafsi kuthibitisha upya dhamira yao ya kuharakisha matumizi ya nishati safi ya kupikia ili kuhakikisha kila kaya nchini inanufaika na suluhisho salama, nafuu na endelevu za kupikia.


Naibu Waziri wa Nishati, Mheshimiwa Salome Makamba (kushoto), akipokewa na Mshauri Mkuu wa Kiufundi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo ya Mitaji (UNCDF), Bw. Peter Malika, kabla hajazindua Kongamano la Kitaifa siku mbili la Nishati Safi ya Kupikia, lililoanza jijini Arusha leo. Kongamano hilo likiwa na kauli mbiu, "Kuendeleza Mustakabali wa Nishati Safi ya Kupikia Tanzania: Mafanikio, Ushirikiano na Njia za Kufikia Asilimia 80 ya Matumizi ifikapo 2034," linaangazia umuhimu wa kuoanisha sera, ufadhili na mikakati ya ushirikishwaji wa jamii ili kuharakisha maendeleo. Kongamano hilo limeandaliwa na UNCDF kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania, kupitia Wizara ya Nishati, kwa msaada wa Umoja wa Ulaya (EU). Wa pili kushoto ni Mkurugenzi wa Nishati Safi ya Kupikia, Wizara ya Nishati, Nolasco Mlay na kulia ni Mwakilishi kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Polycarp Nkuyumba


Mshauri Mkuu wa Kiufundi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo ya Mitaji (UNCDF), Bw. Peter Malika (wa pili kuia), akizungumza wakati wa Kongamano la Kitaifa la siku mbili la Nishati Safi ya Kupikia, lililoanza leo jijini Arusha. Kongamano hilo likiwa na kauli mbiu, "Kuendeleza Mustakabali wa Nishati Safi ya Kupikia Tanzania: Mafanikio, Ushirikiano na Njia za Kufikia Asilimia 80 ya Matumizi ifikapo 2034," linaangazia umuhimu wa kuoanisha sera, ufadhili na mikakati ya ushirikishwaji wa jamii ili kuharakisha maendeleo. Katikati ni Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba na wa pili kushoto ni Balozi wa Umoja wa Ulaya (EU), nchini Tanzania na Jumuiya ya Afrika Mashariki, Bi. Christine Grau.


Naibu Waziri wa Nishati, Mheshimiwa Salome Makamba, akizindua Kongamano la Kitaifa la siku mbili la Nishati Safi ya Kupikia, lililoanza leo jijini Arusha. Kongamano hilo likiwa na kauli mbiu, "Kuendeleza Mustakabali wa Nishati Safi ya Kupikia Tanzania: Mafanikio, Ushirikiano na Njia za Kufikia Asilimia 80 ya Matumizi ifikapo 2034," linaangazia umuhimu wa kuoanisha sera, ufadhili na mikakati ya ushirikishwaji wa jamii ili kuharakisha maendeleo.
Balozi wa Umoja wa Ulaya (EU) nchini Tanzania na Jumuiya ya Afrika Mashariki, Bi. Christine Grau, akizungumza wakati wa Kongamano la Kitaifa la siku mbili la Nishati Safi ya Kupikia jijini Arusha leo. Kongamano hilo limeandaliwa na UNCDF kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania, kupitia Wizara ya Nishati, kwa msaada wa EU.

Naibu Waziri wa Nishati, Mheshimiwa Salome Makamba (wa tatu kutoka kushoto), akipewa maelezo kuhusu faida ya matumizi ya majiko bora ya kupikia na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Burnstove Manufacturing, Bi. Lucia Petro (kulia), wakati wa Kongamano la Kitaifa la Nishati Safi ya Kupikia jijini Arusha leo.

Baadhi ya washiriki wa Kongamano la Kitaifa la siku mbili la Nishati Safi ya Kupikia, lililoanza leo jijini Arusha wakiwa katika kongamano hilo lililoandaliwa na Shirila la Umoja wa Mataifa la Maendeleo ya Mitaji (UNCDF), kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania, kupitia Wizara ya Nishati, kwa msaada wa Umoja wa Ulaya (EU).


Na Mwandishi Wetu

UJUMBE wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania umeungana na mataifa mengine katika Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Kupinga Utumikishwaji wa Mtoto yaliyofanyika Juni 9, 2026 katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, Geneva, Uswisi.

Aidha, ujumbe huo wa Tanzania uliongozwa na Kamishna wa Kazi, Suzan Mkangwa ambaye aliambatana na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Dkt. Yose Joseph Mlyambina, Kamishna wa Kazi Zanzibar, Rashid Khamis Othman, Wakuu wa Taasisi zilizo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano, Wataalamu na Wawakilishi wa Waajiri (ATE) pamoja na Wawakilishi kutoka Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (TUCTA).

Akizungumza wakati wa hafla ya ufunguzi wa maadhimisho hayo, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Kazi Duniani (ILO), Gilbert F. Houngbo ametoa wito kwa jamii ya Kimataifa na Wadau wa Utatu kutekeleza kwa vitendo Mipango na Maadhimio ya Mkutano wa Marrakesh uliofanyika nchini Morocco, Februari 2026 kwa lengo la kupinga utumikishwaji wa Mtoto.

Pia alisisitiza juu ya jitihada za makusudi zinazotakiwa kuchukuliwa na nchi wanachama wa ILO, katika kukuza kazi za staha na utekelezaji wa sera ya elimu bure.

Kwa upande wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mhe. Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano imeendelea kudhihirisha mafanikio yaliyopatikana katika sekta ya kazi na ajira, hasa hatua madhubuti zilizochukuliwa katika kutokomeza ajira za watoto nchini ni kama zifuatazo:- Utekelezaji wa Mradi wa pamoja kati ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Brazil kwa kushirikiana na ILO mradi huo umefanikiwa kwa kiasi kikubwa kutoa elimu kuhusu utumikishwaji wa mtoto na madhara yake.

Pia, kuhuishwa kwa Mkakati wa Taifa wa Kutokomeza Utumikishwaji wa Mtoto 2024/25–2028/29, unaolenga kuunganisha nguvu za wadau wote wa maendeleo, mashirika ya kiraia na jamii kwa ujumla. Kadhalika, Serikali imeendelea kuimarisha mifumo ya Haki Kazini kupitia Mahakama Kuu, Divisheni ya Kazi, na Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA).

Vyombo hivi vimekuwa vikitimiza vyema wajibu wake wa kutafsiri sheria na kutoa haki, hususani ulinzi kwa mtoto; Kuadhimisha Siku ya Kupinga Utumikishwaji wa Mtoto Kitaifa kila tarehe 12 Juni. Wadau kutoka Tanzania Bara na Zanzibar hushiriki na kupokea mikakati ya Serikali ya kukabiliana na tatizo hili; pamoja na Kutoa elimu kwa Umma kwa kuwa utumikishwaji wa mtoto ni jukumu la jamii nzima,

Hivyo ushirikiano baina ya Wizara, wadau wa maendeleo, kaya, na kila mwananchi unahitajika ili kufafanua tafsiri ya utumikishwaji wa mtoto, kazi za shuruti, na kazi hatarishi kwa afya na maendeleo ya mtoto.

Siku ya Kupinga Utumikishwaji wa Mtoto uadhimishwa kila mwaka tarehe 12 Juni na Shirika la Kazi Duniani (ILO) pamoja na nchi wanachama kwa lengo la kuhamasisha nguvu ya pamoja baina ya Serikali, Vyama vya Waajiri, na Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi katika kukuza ajira zenye staha na kutokomeza utumikishwaji wa watoto unaowanyima fursa za kijamii, hususan haki ya elimu.

Maadhimisho hayo kwa mwaka huu 2026 yataongozwa na Kaulimbiu isemayo: “Red Card to Child Labour” ikimaanisha wito kwa wadau wote wa maendeleo kutoonesha uvumilivu wowote kwa vitendo vinavyochochea au kusababisha utumikishwaji wa mtoto katika sekta zote za kijamii na kiuchumi.








Na Mwandishi Wetu

KAMPUNI ya Kitanzania ya Ngoteya Wild, inayoongozwa na muandaaji wa makala zenye maudhui ya uhifadhi na wanyamapori   @Hans_Cosmas_Ngoteya, imetangaza kuwa filamu yao mpya ya Sentinels of Engaruka  ambayo wamefanya kwa kushirikiana na African people and wildlife itaoneshwa rasmi kupitia YouTube channel yao Juni 21, 2026.

Filamu hiyo imechukua zaidi ya miaka mitatu kuandaliwa, ikihusisha utafiti wa kina, upigaji picha wa mazingira ya asili na simulizi inayoonesha uhusiano wa kipekee kati ya jamii ya Kimasai, twiga na mazingira ya Engaruka mkoani Arusha. 

Toleo la Kiswahili la filamu hiyo limesimuliwa na mtangazaji maarufu Meena Ally, ambaye sauti yake itaongeza mguso wa kipekee katika kuifikisha hadithi hiyo kwa watazamaji wa Tanzania na Afrika Mashariki.

Kwa mujibu wa Hans Ngoteya, filamu hiyo inalenga kuhamasisha uhifadhi wa maliasili, kuonesha utajiri wa urithi wa Tanzania na kuifikisha hadithi ya Engaruka kwa hadhira ya kimataifa kupitia jukwaa la YouTube.

Sentinels of Engaruka ni moja ya miradi mikubwa ya filamu za uhifadhi iliyotayarishwa nchini Tanzania, ikiwa na lengo la kuonesha namna jamii na wanyamapori wanavyoweza kuishi kwa maelewano huku wakilinda mazingira kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.




Tume ya Utumishi wa Umma inatarajia kufanya Mkutano wake Na. 4 wa mwaka wa fedha 2025/2026 kuanzia tarehe 15 Juni hadi 3 Julai 2026 jijini Mwanza, ambapo itajadili na kutoa maamuzi kuhusu rufaa na malalamiko mbalimbali yaliyowasilishwa na watumishi wa umma.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma tarehe 10 Juni 2026, Kaimu Katibu wa Tume ya Utumishi wa Umma, Bw. John C. Mbisso, amesema kuwa kupitia mkutano huo, Tume itatoa fursa kwa warufani na warufaniwa walioomba kufika mbele ya Tume ili kutoa ufafanuzi wa ziada kuhusu hoja zilizowasilishwa katika rufaa zao.

Bw. Mbisso amesema hatua hiyo inatekelezwa kwa mujibu wa Kanuni ya 62(1) ya Kanuni za Utumishi wa Umma za mwaka 2022, aidha Tume itapitia taarifa mbalimbali za utekelezaji wa majukumu yake katika kipindi cha robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2025/2026.

Pamoja na shughuli za mkutano, amesema Tume itafanya ziara katika baadhi ya taasisi za serikali zilizopo jijini Mwanza kwa lengo la kutoa elimu kwa waajiri, mamlaka za ajira na mamlaka za nidhamu kuhusu umuhimu wa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu katika usimamizi wa rasilimali watu.

Vilevile ameeleza kuwa Tume itatoa elimu kwa watumishi wa umma katika taasisi hizo kuhusu haki na wajibu wao katika utekelezaji wa majukumu ya utumishi wa umma Sambamba na hilo, itapokea na kushughulikia malalamiko ya watumishi wa umma ambao hawakuridhika na maamuzi yaliyotolewa na waajiri, mamlaka za ajira au mamlaka za nidhamu.

Kwa mujibu wa Kifungu cha 12(1)(d) kikisomwa pamoja na Kifungu cha 27(1)(b) cha Sheria ya Utumishi wa Umma, Sura ya 298, Marejeo ya Mwaka 2023, Tume ya Utumishi wa Umma imepewa mamlaka ya kupokea na kushughulikia rufaa na malalamiko ya watumishi wa umma wasiokubaliana na maamuzi yaliyotolewa na waajiri, mamlaka za ajira na mamlaka za nidhamu katika utumishi wa umma.



Na Karama Kenyunko Michuzi Tv 

KAMPUNI za Singapore zimeendelea kuimarisha uwekezaji wake nchini Tanzania huku kampuni ya Wilmar Rice iliyopo Morogoro ikitajwa kuwa kiwanda kikubwa zaidi cha kusindika mpunga na kuzalisha mchele si Tanzania pekee wala Afrika Mashariki, bali katika bara lote la Afrika.

Akizungumza katika Jukwaa la Biashara la Tanzania na Singapore, Juni 9, 2026 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo amesema uwepo wa wawekezaji wa Singapore nchini unaonyesha namna ushirikiano wa kiuchumi kati ya mataifa hayo mawili unavyoendelea kukua.

"Wilmar Rice Morogoro ni kiwanda kikubwa zaidi cha kusindika mpunga na kuzalisha mchele si Tanzania pekee, si Afrika Mashariki pekee, bali kikubwa zaidi Afrika, na tunajivunia sana kampuni hii iliyopo Morogoro," amesema.

Profesa Mkumbo amesema pamoja na Wilmar Rice, kampuni ya Norman Gohines imekuwa mwekezaji muhimu Zanzibar kwa zaidi ya miaka 100 ikijikita katika uzalishaji wa viungo na shughuli za mashamba ya viungo.

Amesema kampuni hizo ni sehemu ya uwekezaji wa Singapore nchini Tanzania, huku kampuni nyingine nyingi kutoka taifa hilo zikiendelea kufanya shughuli zake nchini.

Profesa Mkumbo amesema Singapore imepitia safari ya maendeleo inayovutia dunia, ikitoka kuwa nchi ndogo yenye kipato cha chini na pato la mtu mmoja mmoja la dola 565 hadi kufikia zaidi ya dola 100,000 kwa sasa.

Amesema mafanikio hayo yameifanya Singapore kuwa na sauti muhimu katika uchumi, diplomasia na siasa za dunia.

Kwa mujibu wa Profesa Mkumbo, kampuni za Singapore ni miongoni mwa wawekezaji wakubwa duniani zikiwa zimewekeza takribani dola trilioni 1.5 katika maeneo mbalimbali duniani, hasa Asia, huku uwekezaji wake barani Afrika ukifikia kati ya dola bilioni 26 na 32 kupitia kampuni takribani 100 zinazofanya shughuli katika nchi 40.

Amesema ziara ya Rais wa Singapore, Tharman Shanmugaratnam, nchini Tanzania itasaidia kupeleka ushirikiano wa kiuchumi kati ya nchi hizo mbili katika hatua nyingine.

Profesa Mkumbo amesema mwelekeo wa kiuchumi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuimarisha ushirikiano wa kimataifa kwa kuvutia biashara na uwekezaji.

"Ametuelekeza tushirikiane na dunia nzima, tusiende kutafuta misaada bali kutafuta washirika wa biashara na uwekezaji," ameisema.

Ameongeza kuwa historia ya maendeleo ya Singapore inatoa mafunzo muhimu ambayo Tanzania inaweza kujifunza na kuyatumia kwa kuzingatia mazingira yake katika safari ya maendeleo.




Na Janeth Raphael MichuziTv

Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa, amesema Bajeti ya Serikali ya mwaka wa fedha 2026/27 ni ya kipekee kwa kuwa ndiyo bajeti ya kwanza kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (2026/27–2030/31) pamoja na Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2025.

Akizungumza jijini Dodoma Juni 10, 2026, amesema bajeti hiyo inalenga kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi.

Balozi Mussa amesema kabla ya kuwasilisha bajeti hiyo bungeni Juni 11, 2026, Bunge litapokea taarifa ya hali ya uchumi wa mwaka 2025 na mwelekeo wake kwa mwaka 2026. Taarifa hiyo itaeleza mwenendo wa uchumi mkuu wa nchi ikiwemo ukuaji wa Pato la Taifa (GDP), mfumuko wa bei, biashara ya nje na kiwango cha akiba ya fedha za kigeni.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, Serikali inapanga kutumia Shilingi trilioni 62.3 katika mwaka wa fedha 2026/27, ambapo fedha nyingi zitaelekezwa kwenye miradi ya maendeleo na huduma muhimu kwa wananchi. Matumizi hayo yanatarajiwa kufadhiliwa kwa kiasi kikubwa na mapato ya ndani yatakayofikia Shilingi trilioni 46.8, hatua inayodhihirisha kuongezeka kwa uwezo wa nchi kujitegemea katika kugharamia maendeleo yake.

Amesema miradi ya kimkakati itakayopewa kipaumbele ni pamoja na ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR), upanuzi wa miundombinu ya barabara, miradi ya maji, nishati pamoja na maendeleo ya rasilimali watu na ujuzi. Aidha, alibainisha kuwa Serikali imeendelea kufanya vizuri katika ukusanyaji wa mapato ya ndani na kufikia malengo yaliyowekwa katika mwaka wa fedha 2025/26.

Kuhusu maboresho ya kodi, ada na tozo, Waziri Mussa alisema Serikali ilipokea mapendekezo 727 kutoka kwa wadau mbalimbali wakiwemo taasisi za Serikali, sekta binafsi, wafanyabiashara, taasisi za elimu, mashirika yasiyo ya kiserikali na wananchi. Kati ya hayo, mapendekezo 125 yalikubaliwa moja kwa moja, 121 yaliboreshwa na kukubaliwa huku 295 yakikataliwa, na mengine kupelekwa kwa uchambuzi zaidi.

Amesema ushirikishwaji wa wadau pamoja na ushauri wa Kamati ya Wataalam wa Maboresho ya Kodi na kamati ya kiufundi ya “Think Tank” umesaidia kupata mawazo yatakayoboa mfumo wa kodi, kuvutia uwekezaji, kuongeza ajira na kuimarisha ukusanyaji wa mapato. Aliwataka Watanzania kuendelea kulipa kodi kwa hiari na kufuatilia kwa karibu uwasilishaji wa Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2026/27 utakaofanyika bungeni Juni 11, 2026.


Na Said Mwishehe,Michuzi TV

RAIS wa Singapore, Tharman Shanmugaratnam, amesema kwamba ndoto ya Tanzania kufikia uchumi wa thamani ya dola trilioni moja ifikapo mwaka 2050 inategemea utekelezaji wa haraka wa mageuzi katika elimu, nishati ya umeme na utawala wa serikali.

Akizungumza katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam wakati wa mhadhara wa wazi uliondaliwa kwa ushirikiano wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,Taasisi ya Uongozi pamoja na chuo hicho Rais Tharman amesema ukuaji wa taifa unategemea kujenga rasilimali watu imara na kuhakikisha kwamba elimu inayotolewa shuleni inaendana na mahitaji halisi ya soko la ajira.

Amebainisha Afrika inakabiliwa na mabadiliko makubwa ya idadi ya watu. Kwa kuwa mamia ya mamilioni ya vijana wanatarajiwa kuingia kwenye soko la ajira katika kipindi kijacho, uundaji wa nafasi za kazi ni jambo la dharura.

Aidha amesema mwenendo wa sasa unaweza kusababisha pengo kubwa kati ya wanaotafuta ajira na nafasi za kazi zinazopatikana.“Hili si pengo la idadi pekee, bali ni pengo la matumaini na fursa.”

Ili kutatua changamoto hiyo, amesema pia shule zinapaswa kuacha kuzingatia vyeti pekee na badala yake kujikita katika ujuzi wa vitendo, ushirikiano wa kikazi na kujifunza kwa maisha yote.

Ametoa mwito wa kuongeza uwekezaji katika elimu ya ufundi na mafunzo ya stadi za kazi (TVET) ili kupunguza tofauti kubwa ya ujuzi unaohitajika na unaopatikana.

Rais Tharman ameongeza mafunzo ya ujuzi yanapaswa kuunganishwa moja kwa moja na maendeleo ya miundombinu, ukuaji wa teknolojia ya kidijitali na sera za biashara ili kusaidia sekta binafsi kuzalisha ajira.

Kuhusu nishati, Tharman amesema kuwa umeme ndiyo injini kuu ya maendeleo ya viwanda na kufafanua upatikanaji hafifu wa umeme bado ni kikwazo kikubwa kwa mataifa mengi ya Afrika.

Ametumia nafasi hiyo kuihimiza Tanzania kuhamia kwenye nishati safi ili kuimarisha mifumo ya umeme, kuvutia wawekezaji wa kimataifa na kupunguza utegemezi wa mifumo ya zamani yenye gharama kubwa.

Pia amesisitiza umuhimu wa kujenga na kuboresha njia za usafirishaji wa umeme na miundombinu ya gridi za taifa.

Kuhusu biashara, Tharman alihimiza kuimarishwa kwa ushirikiano na Eneo Huru la Biashara la Bara la Afrika (AfCFTA). Alisema kuwa mgawanyiko wa masoko unaathiri ukuaji wa kampuni za ndani.

Alieleza kuwa soko la pamoja lingeziwezesha biashara za Tanzania kupanuka zaidi katika sekta za viwanda, kilimo na huduma.Pia utawala bora na sheria zinazotabirika ni muhimu katika kuvutia uwekezaji wa muda mrefu kutoka nje ya nchi.

Akirejea takwimu za IMF, amebainisha kuwa kupunguza rushwa na kuongeza uwazi kunaweza kuchochea kwa kiasi kikubwa ukuaji wa uchumi katika nchi za Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara.

Kwa upande wake Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo, amesema ziara hiyo ni hatua muhimu inayoonyesha kuimarika kwa uhusiano kati ya mataifa hayo mawili.“Mafanikio ya Singapore yanatoa mafunzo muhimu kuhusu nidhamu na mipango ya muda mrefu.”

Wakati huo huo Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa William Anangisye, amesema chuo hicho kinajivunia kuwa mwenyeji wa hotuba hiyo, akisisitiza mchango wake katika kuwaandaa vijana kufikia malengo ya maendeleo ya taifa.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Taasisi ya Uongozi, Balozi Ombeni Sefue, ameongeza kuwa mafanikio ya Singapore yanaonyesha kwamba maendeleo yanatokana na uongozi bora na taasisi imara, si rasilimali za asili pekee.

Alihitimisha kwa kueleza kuwa mustakabali wa Afrika unategemea ubunifu wa ndani na utawala bora imara.


Na Said Mwishehe,Michuzi TV

RAIS wa Singapore Tharman Shanmugaratnam amesema kwamba maendeleo ya ujuzi, upanuzi wa nishati, taasisi imara na ujumuishaji wa kifedha kuwa maeneo muhimu ambayo Tanzania inapaswa kuyaimarisha ili kutekeleza kwa mafanikio Dira ya Taifa ya 2050.

Ameyasema hayo alipokuwa akizungumza katika mhadhara wa wazi uliofanyika jana katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, wenye mada “Kuwekeza katika Vichocheo vya Ukuaji Jumuishi”,

Mhadhara huo wa wazi umeandaliwa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushiriano wa Afrika Mashariki,Taasisi ya Uongozi pamoja na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam(UDSM) ambapo Rais Tharman ametumia nafasi hiyo kueleza kwamba Tanzania ina misingi imara ya ukuaji wa baadaye, ikiwemo idadi kubwa ya vijana, rasilimali nyingi za asili na utulivu wa kisiasa.

Amefafanua kuwa kugeuza faida hizo kuwa ustawi endelevu kutahitaji uwekezaji wa makusudi katika rasilimali watu, miundombinu na taasisi zenye ufanisi huku elimu na maendeleo ya ujuzi vinapaswa kubaki kuwa kiini cha ajenda ya maendeleo ya Tanzania, akieleza kuwa nchi zitakazofanikiwa katika siku zijazo ni zile zinazowekeza daima kwa watu wake.

“Mifumo ya elimu lazima iwaandae vijana kwa soko la ajira ambalo linaendelea kubadilishwa na maendeleo ya teknolojia, otomatiki (automation) na akili mnemba (Artificial Intelligence), huku pia ikitoa fursa kwa wafanyakazi kuendelea kuboresha ujuzi wao katika maisha yao ya kazi.”

Pia ameitaja nishati ya uhakika na yenye gharama nafuu kuwa kichocheo muhimu cha mabadiliko ya kiuchumi na kusisitiza uendelezaji wa viwanda, matumizi ya teknolojia za kidijitali na uundaji wa ajira vinategemea upatikanaji wa nishati ya kutosha, hivyo kufanya uwekezaji katika uzalishaji na usambazaji wa umeme kuwa muhimu kwa ukuaji wa muda mrefu.

“Taasisi imara na utawala bora pia ni muhimu katika kufikia maendeleo endelevu.Pia uthabiti wa sera, uwazi na imani ya wananchi husaidia kujenga mazingira yanayovutia uwekezaji, kuhimiza ubunifu na kuhakikisha manufaa ya ukuaji wa uchumi yanawanufaisha wananchi wengi,”amesema.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa ujumuishaji wa kifedha kama sehemu muhimu ya maendeleo ya kiuchumi, akibainisha kuwa upatikanaji mpana wa huduma za kifedha unaweza kuziwezesha kaya, kusaidia ujasiriamali na kupanua fursa za kiuchumi.

Pia ameeleza umuhimu wa ushirikiano kati ya serikali na sekta binafsi, akisema mikakati yenye mafanikio ya maendeleo inahitaji ushirikiano unaoweza kuhamasisha mtaji, teknolojia na utaalamu.

Kwa upande wake Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mahmoud Thabit Kombo, amesema mhadhara huo umeakisi ushirikiano unaozidi kuimarika kati ya Tanzania na Singapore wakati nchi hizo mbili zikiadhimisha miaka 45 ya uhusiano wa kidiplomasia.

“Tanzania inathamini uzoefu wa Singapore katika maendeleo na inaona fursa kubwa za kuimarisha ushirikiano katika biashara, uwekezaji, utawala wa umma, maendeleo ya ujuzi na mageuzi ya kiuchumi.”

Awali Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa William Anangisye, amesema taasisi hiyo imeheshimiwa kuwa mwenyeji wa mhadhara huo, akiueleza kuwa ni jukwaa muhimu la kubadilishana mawazo kuhusu ukuaji jumuishi na maendeleo ya taifa.

“Mawazo na uzoefu wa Rais Tharman utachangia mijadala inayoendelea kuhusu matarajio ya maendeleo ya muda mrefu ya Tanzania na utekelezaji wa Dira ya 2050.”

Mhadhara huo wa wazi ulikuwa sehemu ya ziara ya kiserikali ya siku tatu ya Tharman nchini Tanzania.














Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, ameieleza Jumuiya ya Kimataifa hatua kubwa zinazochukuliwa na Serikali ya Tanzania katika kulinda na kuendeleza haki za watu wenye ulemavu, wakati aliposhiriki Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19) unaofanyika katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, Jijini New York, Marekani.

Mhe. Mahundi, ambaye amemuwakilisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu–Sera, Bunge na Uratibu  na Wenye Ulemavu, Mhe. Profesa Palamagamba John Kabudi, amesema Tanzania imeendelea kuimarisha mifumo ya kisheria, kisera na kiutendaji ili kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata haki, fursa na huduma stahiki kama wananchi wengine.

Akiwasilisha taarifa ya nchi, Mhe. Mahundi amesema Tanzania imepiga hatua kubwa kupitia Sheria ya Watu Wenye Ulemavu Na. 9 ya mwaka 2010 kwa Tanzania Bara pamoja na Sheria Na.8 ya mwaka 2022 ya Zanzibar, ambazo zimeweka msingi imara wa kulinda haki na ustawi wa watu wenye ulemavu.

 “Masuala ya ulemavu yamejumuishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na mipango mbalimbali ya maendeleo ili kuhakikisha hakuna anayebaki nyuma katika safari ya maendeleo ya taifa na kusema kuwa Serikali imeendelea kupanua upatikanaji wa elimu jumuishi, huduma za afya, huduma za urekebishaji na tiba, teknolojia saidizi, programu za uwezeshaji kiuchumi pamoja na huduma za hifadhi ya jamii kwa watu wenye ulemavu” @maryprisca_mahundi.

Aidha  Mhe. Mahundi amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa uongozi wake madhubuti na dhamira ya dhati ya kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata huduma bora na fursa zinazowawezesha kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya nchi.

Mkutano huo wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu umebeba kaulimbiu inayosema “CRPD at 20: Celebrating and Consolidating Achievements and Shaping the Next Phase of Implementation in a Changing World,” ukilenga kutathmini mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 20 tangu kuanzishwa kwa mkataba huo na kuweka mikakati.







Bohari ya Dawa (MSD) imeihakikishia Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI kuwa itaendelea kuimarisha upatikanaji wa bidhaa za afya zenye ubora, kwa wakati na kwa kiwango kinachohitajika kuelekea utekelezaji wa awamu ya pili ya Bima ya Afya kwa Wote.

Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi Mkuu wa MSD, Mavere Tukai, mbele ya Kamati hiyo Juni 9, 2026 mara baada ya wajumbe wa Kamati hiyo kufanya ziara katika Ghala Kuu la MSD Dodoma kwa lengo la kujionea shughuli za kila siku za taasisi hiyo katika uzalishaji, ununuzi, uhifadhi na usambazaji wa bidhaa za afya.

“Sisi tumeshajipanga, na utayari wetu unategemea kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa rasilimali. Tayari tumewasilisha mahitaji yetu Serikalini kwa ajili ya kuwezesha utekelezaji wa mpango wa Bima ya Afya kwa Wote na kuhakikisha wananchi wanapata huduma zinazostahili,” amesema Mavere.

Amesema MSD inaendelea kujiandaa kukidhi ongezeko la mahitaji ya bidhaa za afya litakalotokana na utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote, huku akibainisha kuwa bidhaa za afya zenye thamani ya zaidi ya Shilingi trilioni 1.2 hununuliwa kupitia MSD na kusambazwa katika vituo vya kutolea huduma za afya nchini.

Katika ziara hiyo, wajumbe wa Kamati walipata maelezo kuhusu mifumo ya ugavi wa bidhaa za afya, hatua zinazochukuliwa kuhakikisha upatikanaji wa bidhaa hizo nchini pamoja na mifumo ya udhibiti wa ubora inayotekelezwa kwa kushirikiana na mamlaka mbalimbali ikiwemo Mamlaka ya Dawa na VifaaTiba (TMDA) na taasisi nyingine za ndani na nje ya nchi.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI, Mhe. Johannes Lukumay, ameipongeza MSD kwa kazi kubwa inayofanya ya kuhakikisha wananchi wanapata bidhaa za afya zenye ubora na kwa wakati, huku akiitaka taasisi hiyo kuendelea kuimarisha mifumo yake ili kukidhi mahitaji yanayoongezeka ya huduma za afya nchini.

Naye Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Dkt. Zeyana Abdallah Hamid, ameutaka uongozi wa MSD kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu shughuli za taasisi hiyo ili wananchi waweze kufahamu thamani ya uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali katika kuhakikisha bidhaa za afya zinapatikana kwa uhakika nchini.









Top News