Benki ya Exim Tanzania imeingia katika ushirikiano wa kimkakati na Toyota wenye lengo la kufanya umiliki wa magari kuwa rahisi zaidi na nafuu kwa Watanzania.

Kupitia ushirikiano huu, suluhisho maalum la ufadhili wa magari limeanzishwa, likiwwawezesha watu binafsi na biashara kununua magari mapya na yaliyotumika kwa gharama ndogo ya awali Pamoja na muda nafuu wa marejesho unaoweza kufikia hadi miaka sita.

Akizungumza wakati wa hafla ya utiaji Saini huo, Mkuu wa Huduma za Benki kwa Wateja Binafsi na wa Kati wa Benki ya Exim Tanzania, Andrew Lyimo, alisema ushirikiano huo unaonesha dhamira ya Benki kuendelea kutoa suluhisho bunifu na zinazomlenga mteja moja kwa moja.

“Katika Benki ya Exim Tanzania, tunalenga kufanya zaidi ya huduma za Kibenki za kawaida kwa kutoa suluhisho zinazogusa mahitaji halisi ya kila siku ya wateja wetu. Ushirikiano huu na Toyota unatupa fursa ya kurahisisha umiliki wa magari kupitia mipango nafuu ya ufadhili inayopunguza mzigo wa kifedha huku ikiunga mkono mahitaji ya usafiri binafsi na ukuaji wa biashara,” alisema Lyimo.

Kupitia mpango huu, Benki ya Exim itatoa ufadhili wa hadi asilimia 80 ya gharama kwa magari mapya na asilimia 70 kwa magari yaliyotumika, kwa viwango vya riba shindani vinavyokokotolewa kwa mfumo wa salio linalopungua. Huduma hii inapatikana kwa Shilingi za Kitanzania na Dola za Marekani, ikiwa na malipo ya awali kuanzia asilimia 20.

Kifurushi hiki cha ufadhili wa magari kimetengenezwa ili kuwahudumia wateja mbalimbali wakiwemo waajiriwa, wajasiriamali, biashara ndogo na za kati (SMEs), pamoja na makampuni yanayohitaji suluhisho la uhakika la usafiri bila kuathiri mtiririko wa fedha.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Toyota, Meneja Mkuu William Kadiva, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano huo katika kupanua upatikanaji wa magari yenye ubora nchini Tanzania.

“Ushirikiano wetu na Benki ya Exim Tanzania ni hatua muhimu katika kuhakikisha magari ya Toyota yanawafikia Watanzania wengi zaidi. Kwa kuunganisha ubora wa magari yetu na suluhisho nafuu za ufadhili, tunawezesha watu wengi zaidi kumiliki magari yanayotegemewa kwa matumizi ya kila siku na shughuli za kibiashara,” alisema Kadiva.

Wateja wanaweza kupata huduma hii kwa kutembelea tawi lolote la Exim Bank au showroom za Toyota (Automark) kote nchini ili kujionea chaguo zilizopo na kuanza safari ya kumiliki gari.

Ushirikiano huu unaakisi dhamira ya pamoja ya Exim Bank na Toyota ya kuchochea shughuli za kiuchumi, kuboresha usafiri, na kuunga mkono ukuaji wa biashara nchini Tanzania.

Kuhusu Exim Bank Tanzania

Ilianzishwa mwaka 1997, Exim Bank Tanzania ni mojawapo ya taasisi zinazoongoza za kifedha nchini, inayotambulika kwa ubunifu wake, suluhisho zinazomlenga mteja, na mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi wa Tanzania. Ikiwa na uwepo imara wa kikanda katika nchi za Comoro, Djibouti, Uganda, na Ethiopia, Exim Bank ni miongoni mwa benki chache za asili ya Tanzania zilizofanikiwa kupanua shughuli zake nje ya mipaka ya nchi.

Kupitia mtandao wake mpana wa matawi na majukwaa ya kisasa ya huduma za benki kidijitali, Exim Bank inaendelea kuwawezesha watu binafsi na biashara kwa huduma za kifedha zilizo thabiti, rahisi kubadilika, na zenye mwelekeo wa maendeleo ya baadaye.


Kuhusu Toyota Tanzania

Toyota Tanzania Ltd, iliyoanzishwa mwaka 1965, ni msambazaji pekee wa magari ya Toyota nchini Tanzania na mdau mkuu katika sekta ya magari. Kampuni hii hutoa aina mbalimbali za magari na huduma. Imeendelea kushikilia nafasi ya uongozi katika soko la magari mapya nchini, kwa kuzingatia uendelevu na kutoa suluhisho bora za usafiri kwa wateja wake.

Mkuu wa Kitengo cha Wateja Binafsi na wa Kati wa Benki ya Exim Tanzania, Bw.Andrew Lyimo( wa pili kushoto) na Meneja Mkuu wa Toyota Tanzania Bw.William Kadiva (wa pili kulia) wakisaini mkataba wa makubaliano ya ushirikiano unaolenga kuwawezesha wateja wake kumiliki gari ya ndoto yake. Hafla hii ilifanyika ofisi za Toyota Tanzania, jijini Dar es Salaam tarehe 21 April 2026, Ikishuhudiwa na Afisa Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania Bw. Stanley Kafu (kushoto) na Mkuu wa Kitengo cha Usimamizi wa Sheria wa Toyota Tanzania Bi. Lucia Minde (kulia).

▪️ Serikali, Chemba ya Migodi Wapanga Mkakati Kabambe Kukuza Uchumi Kupitia Madini

▪️ Waziri Mavunde Asikiliza na Kutatua Changamoto, Maboresho na Kuahidi Kuyafanyia Kazi

▪️ Atoa Onyo Kali kwa wamiliki wa Leseni ambao hawaziendelezi

▪️ Utafiti wa Madini Watajwa Kuwa Injini ya Uchumi wa Madini Kuelekea Uchumi wa Dola Trilioni



Serikali kupitia Wizara ya Madini kwa kushirikiana na Chemba ya Migodi Tanzania (TCM) imejadili na kuweka mikakati wa kuifanya Sekta ya Madini kuwa mhimili mkuu wa kufikia Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 ya kuifanya Tanzania kufikia uchumi wa thamani ya dola trilioni moja ifikapo mwaka 2050, kwa kusisitiza utafiti wa madini, usimamizi madhubuti na ushirikiano na sekta binafsi kama nguzo kuu za mafanikio hayo.

Akizungumza katika kikao na Chemba ya Migodi kilichofanyika katika ukumbi wa Tume ya Madini jijini Dodoma, leo Aprili 21, 2026, Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde amesema kuwa hatua hiyo haiwezekani bila kuwekeza kwa nguvu katika utafiti wa kina wa rasilimali madini kwa kushirikiana na sekta binafsi.

Ameeleza kuwa utafiti wa madini unapaswa kupewa kipaumbele kwani ndio unaofungua milango ya uwekezaji, kuongeza tija na kuhakikisha nchi inanufaika ipasavyo na rasilimali zake.

Katika kikao hicho, Waziri Mavunde amepokea changamoto, maoni na mapendekezo kutoka kwa wadau wa Sekta ya Madini kupitia TCM, akiahidi kuwa Serikali itayafanyia kazi kwa lengo la kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa wanachama wa TCM kupitisha hoja zao kupitia umoja wao ili kuwa na sauti moja yenye nguvu na kurahisisha mawasiliano kati ya Serikali na sekta binafsi.

Kwa upande wa usimamizi, Waziri Mavunde ameelekeza kuimarishwa kwa ushirikiano kati ya Ofisi ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini na taasisi za kiserikali ili kuhakikisha utekelezaji wa Sera na Sheria unakuwa na ufanisi zaidi bila kuingilia na kuleta usumbufu kwa wawekezaji.

Akizungumzia changamoto ya uvamizi wa maeneo yenye leseni halali za uchimbaji, Mavunde amesisitiza kuwa vitendo hivyo havitavumiliwa na tayari maelekezo yametolewa kwa Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa, kupitia Ofisi ya Mtendaji Mkuu wa Tume ya Madini, kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kuwaondoa mara moja wavamizi wote na ametumia nafasi kueleza msimamo wa serikali wa kufuta leseni ambazo hazifanyi kazi zinazomilikiwa na wawekezaji hao.

Amefafanua kuwa Serikali imeanzisha mfumo wa kidijitali unaohakikisha kuwa leseni za utafiti zinazoisha muda wake zinarejeshwa moja kwa moja Serikalini, hatua inayolenga kudhibiti tabia ya watu kushikilia maeneo makubwa kwa matarajio ya kuvutia wawekezaji baadaye.

Katika kuimarisha ajenda ya Ushirikiwa wa Watanzania kwenye sekta ya madini, Waziri Mavunde ameeleza kuwa, kuanzishwa kwa maeneo maalum ya uwekezaji wa viwanda vinavyozalisha vifaa na vipuri vya migodini, akitaja eneo la mgodi wa uliofungwa wa Buzwagi kama kitovu kinachoweza kuendelezwa kuwa ukanda maalum wa uchumi kwa shughuli hizo.

Pia, amekazia kuwa orodha ya bidhaa na huduma 20 zilizotengwa kwa Watanzania pekee katika migodi itaendelea kulindwa bila mabadiliko, akibainisha kuwa Serikali inalenga kulinda maslahi ya wazawa kwa kuzingatia sheria zilizopo.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Madini Steven Kiruswa amesema kuwa pamoja na juhudi za kuvutia wawekezaji, Serikali inaweka mkazo katika madini muhimu na ya kimkakati ambayo yanaendelea kuwa na soko kubwa katika zama za mabadiliko ya teknolojia na mazingira duniani.

Naye, Katibu Mkuu wa TCM, Eng. Benjamin Mchwampaka, ameipongeza Serikali kwa hatua zake za kushughulikia changamoto za sekta hiyo na kudumisha ushirikiano thabiti na sekta binafsi, ameongeza kuwa Serikali inashauriwa kudumisha uthabiti wa Sera, Sheria na moiongozo ya Sekta ya Madini, kwani mabadiliko ya mara kwa mara kwani huchelewesha maamuzi ya uwekezaji na kwamba mazingira ya kisheria yanayotabirika yanaongeza ushindani wa nchi, huvutia uwekezaji wa muda mrefu, na kuhakikisha rasilimali za madini zinachangia kikamilifu ukuaji endelevu wa uchumi.

Kwa upande wa Serikali, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini Eng. Yahya Samamba amebainisha kuwa mpango maalum unaandaliwa kufadhili wataalamu wa Kitanzania kujifunza katika fani za kisasa kama uchumi wa madini (Mineral Economy), ili kuendana na mahitaji pamoja na mabadiliko ya kimataifa na kuongeza ushindani wa nchi.

Kwa ujumla, kikao hicho kimeonesha dhamira ya dhati ya Serikali na wadau wa Sekta ya Madini kujenga msingi imara utakaowezesha sekta hiyo kuwa moja ya injini ya uchumi wa Tanzania kuelekea 2050.








Na Oscar Assenga, Tanga



Kwa muda mrefu, gharama za pango zimekuwa mzigo usioonekana lakini mzito kwa taasisi nyingi nchini.

Ni gharama ambazo zimezoeleka kiasi cha kukubalika kama sehemu ya kawaida ya uendeshaji, bila kuhojiwa kwa kina iwapo zinaweza kubadilishwa kuwa fursa.

Ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Tanga, hali hiyo inaanza kuchukua mwelekeo mpya.

Fedha ambazo zilikuwa zikitumika kila mwaka kugharamia makazi ya watumishi sasa zinaelekezwa kwenye mkakati wenye dira tofauti ujenzi wa nyumba za watumishi katika kila wilaya ya mkoa.

Haya ni mabadiliko kutoka matumizi ya muda mfupi kwenda uwekezaji wa muda mrefu.





Upepo Mpya wa Ubunifu

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga, Rajab Abdurhaman, anauelezea mkakati huo kama hatua ya kimkakati inayolenga kupunguza matumizi yasiyo ya lazima na kuimarisha uwezo wa chama kuwekeza katika maendeleo mengine.

Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua miradi ya chama mkoani humo, ikiwemo ujenzi wa nyumba za watumishi, Abdurhaman alionesha kuridhishwa na hatua nyumba hizo zilizofikiwa katika maeneo mbalimbali mkoani humo , lakini zaidi akisisitiza thamani ya mshikamano uliowezesha mafanikio hayo.

“Kwa ujumla mmefanya kazi kubwa sana. Nawashukuru wadau wote walioshiriki, kwa sababu walichotoa si msaada tu, bali ni uwekezaji ambao utaendelea kuzaa matunda,” alisema kwa msisitizo.

Kauli hiyo inaakisi mwelekeo mpya wa fikra kutazama rasilimali si kama matumizi ya papo kwa papo, bali kama uwekezaji wa muda mrefu.


Kutoka Pango kwenda Uwekezaji

Kabla ya mradi huu kuanza, baadhi ya watumishi walikuwa wakilipa hadi shilingi 200,000 kwa mwezi kama pango, huku wengine wakilipa zaidi kulingana na eneo.

Kwa mwaka mmoja, gharama hizo zilijikusanya na kuwa mzigo mkubwa kwa chama—fedha ambazo, kwa mtazamo wa sasa, zingeelekezwa kwenye miradi mingine ya maendeleo.

Sasa picha inaanza kubadilika.

Kwa makadirio ya haraka, kukamilika kwa nyumba hizo katika wilaya zote za Mkoa wa Tanga kunatarajiwa kuiwezesha CCM kuokoa hadi shilingi milioni 90 kwa mwaka.

Fedha hizo, kwa mujibu wa uongozi wa chama, sasa zinageuka kuwa mtaji mpya wa maendeleo ya ndani.

“Fedha hizi zitasaidia kufanya shughuli nyingine za maendeleo ndani ya chama. Huu ni ubunifu ambao umehimizwa na Mwenyekiti wa CCM Taifa pamoja na Kamati Kuu,” alieleza Abdurhaman.

Zaidi ya Takwimu: Ustawi wa Mtumishi

Licha ya faida za kifedha, mchango mkubwa zaidi wa mradi huu upo katika kuboresha ustawi wa watumishi.

Makazi bora, salama na yenye hadhi yanatarajiwa kuongeza ari, utulivu na ufanisi kazini—ambapo matokeo yake yanaonekana moja kwa moja katika utendaji wa kila siku.

Kwa lugha rahisi, mtumishi mwenye uhakika wa makazi ni mtumishi mwenye uhakika wa kazi bora.
Nidhamu ya Mali na Usimamizi wa Ardhi

Katika hatua nyingine, Abdurhaman alisisitiza umuhimu wa kulinda mali za chama kwa kuhakikisha maeneo yote yana hati miliki halali.

Alibainisha kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kuzuia migogoro ya ardhi na kulinda uwekezaji wa muda mrefu wa chama.

Aidha, alihimiza upandaji wa miti ya kivuli na matunda katika maeneo ya chama, hatua inayolenga si tu kuboresha mazingira bali pia kuongeza thamani ya maeneo hayo na kulinda mipaka yake.






Wajibu wa Viongozi wa Wilaya

Viongozi wa chama katika ngazi ya wilaya wamepewa jukumu la kuhakikisha sheria za ardhi zinazingatiwa kikamilifu, ikiwemo ulipaji wa kodi ya pango la ardhi na kufuata taratibu zote za umiliki.

Hii inaweka msisitizo kwenye uwajibikaji na nidhamu ya matumizi ya mali za umma na za chama.



Hitimisho: Gharama Zinapogeuka Fursa

Kwa ujumla, mkakati wa ujenzi wa nyumba za watumishi unaibuka kama mfano wa namna taasisi zinavyoweza kubadili changamoto kuwa fursa za kiuchumi na kijamii.

Ndani ya CCM Tanga, hatua hii si tu inaboresha maisha ya watumishi, bali pia inaweka msingi imara wa uendelevu wa kifedha na kiutendaji wa chama kwa siku zijazo.

Na zaidi ya yote, inaonesha kwamba maendeleo si suala la kuongeza matumizi—bali ni sanaa ya kuyabadilisha kuwa uwekezaji.

0714543839
Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), leo 21 Aprili 2026, imetumia fursa ya Wiki ya Nishati kuwahamasisha waheshimiwa wabunge kuwekeza katika ujenzi wa vituo vya mafuta maeneo ya vijijini pamoja na vituo vya CNG ili kuendelea kusogeza huduma kwa wananchi.

Kaimu Meneja wa Mawasiliano na Uhusiano wa EWURA, Bw. Wilfred Mwakalosi, alisema kuwa EWURA inatumia maonesho hayo kutoa elimu kuhusu namna inavyohakikisha upatikanaji wa huduma za nishati na maji kwa wakati na kwa gharama nafuu.

Alibainisha kuwa wabunge ni wawakilishi wa wananchi, hivyo kuwajengea uelewa kuhusu udhibiti, fursa za uwekezaji na utaratibu wa kupokea na kushughulikia migogoro na malalamiko kutawawezesha kuwasilisha taarifa sahihi kwa wananchi kuhusu juhudi za Serikali katika kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora za umeme, mafuta na gesi asilia.

Akizungumza katika maonesho hayo, Ofisa Mwandamizi wa Kitengo cha Mafuta, Mha. Ibrahim Kajugusi, alisema elimu inayotolewa pia inalenga kuwafahamisha wananchi jinsi EWURA inavyosimamia upatikanaji wa huduma za mafuta nchini kwa kuzingatia ubora uliopitishwa na gharama sahihi. Aidha, aliwahamasisha wananchi kuchangamkia fursa za uwekezaji katika sekta hiyo, hususan ujenzi wa vituo vya mafuta vya gharama nafuu vijijini na mijini pamoja vituo vya kujazia gesi asilia kwenye magari (CNG).

Kwa upande wake, Bi. Achilana Mtingele, mchumi wa EWURA, alisema elimu inayotolewa imejikita katika kueleza namna EWURA inavyosimamia upangaji wa viwango vya bei za huduma za umeme, mafuta na gesi asilia. Aliongeza kuwa mamlaka hiyo huweka mizania kati ya maslahi ya watoa huduma na watumiaji, na kwamba wabunge waliopata elimu hiyo wataweza kuiwasilisha ipasavyo kwa wananchi katika maeneo yao.

Akizungumzia sekta ya gesi asilia, Mhandisi Mwandamizi wa Gesi Asilia, Mha. Evaline Rweikiza, alisema EWURA itaendelea kusimamia ubora wa miundombinu ya gesi asilia nchini na kuhamasisha matumizi yake, hususan katika magari. Alibainisha kuwa hadi sasa vituo 18 vimepata leseni ya EWURA kutoa huduma ya gesi asilia, huku vituo sita vingine vikiwa katika hatua za mwisho za kupata leseni katika mikoa ya Dar es Salaam na Pwani. Aidha, mipango inaendelea kwa baadhi ya makampuni kusambaza gesi asilia iliyokandamizwa katika mikoa ya Morogoro na Dodoma.

Kwa upande wa sekta ya umeme, Mhandisi Mwandamizi wa Umeme, Lulu Chilumba, aliwahamasisha wabunge na wadau wanaotembelea maonesho hayo kutumia mafundi umeme wenye leseni kutoka EWURA ili kuhakikisha usalama wa nyumba na mali zao. Alisema EWURA inaendelea kutoa leseni kwa mafundi umeme wenye sifa stahiki, ambapo zaidi ya leseni 1,000 zilitolewa katika mwaka wa fedha uliopita.

Naye Ofisa Rasilimali Watu Mkuu, Bi. Limi Kahabi, alisema EWURA ni mwajiri anayezingatia misingi ya usawa na haki katika mchakato wa ajira, akisisitiza kuwa taasisi hiyo huajiri kwa kuzingatia sifa, weledi na usawa kwa wote.


Watu kadhaa wamefariki dunia na wengine kujeruhiwa baada ya basi la abiria kugongana uso kwa uso na lori katika eneo la Mlima “S”, kijiji cha Lumango, wilayani Kilosa mkoani Morogoro.

Ajali hiyo ilihusisha basi la kampuni ya ZL Super Safari lililokuwa likitoka Ifakara kuelekea Morogoro, pamoja na lori lililokuwa limebeba kokoto.

Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo, chanzo cha ajali kinadaiwa kuwa ni uzembe wa dereva wa lori aliyekuwa akijaribu bajaji iliyokuwa mbele yake, hali iliyosababisha kugongana na basi hilo.

Juhudi za kumpata Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro ili kuzungumzia tukio hilo zinaendelea.

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndg. Asha-Rose Migiro, leo tarehe 21 Aprili 2026 amekutana na kufanya mazungumzo na ujumbe wa Mtandao wa Viongozi Wanawake wa Afrika (African Women Leaders Network - AWLN), ulioongozwa na Marais wastaafu wa Jamhuri ya Liberia, Mhe. Ellen Johnson Sirleaf, na Jamhuri ya Shirikisho la Kidemokrasia ya Ethiopia, Mhe. Sahle-Work Zewde, jijini Dar es Salaam.

Mazungumzo hayo yalijikita katika hali ya kisiasa nchini pamoja na matukio ya wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025, yakihusisha pia umuhimu wa kudumisha amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa.

Ujumbe huo upo nchini Tanzania kwa ziara ya kikazi yenye lengo la kufanya mashauriano na viongozi mbalimbali wa kitaifa kuhusu maendeleo ya kisiasa na juhudi zinazoendelea za kuimarisha demokrasia na utawala bora, ikiwa ni sehemu ya mchango wa wanawake viongozi wa Afrika katika kulinda amani na utulivu barani.






Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akitoa heshima za mwisho kwa mwili wa Askofu wa Jimbo Katoliki Kondoa, marehemu Askofu Bernadin Francis Mfumbusa, mara baada ya Ibada ya kumuaga na kumuombea iliyofanyika Katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Paulo wa Msalaba , Jimbo Kuu Katoliki Dodoma, leo tarehe 21 Aprili 2026.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akiwasili Katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Paulo wa Msalaba , Jimbo Kuu Katoliki Dodoma, kushiriki Ibada ya kumuaga na kumuombea Askofu wa Jimbo Katoliki Kondoa, marehemu Askofu Bernadin Francis Mfumbusa, leo tarehe 21 Aprili 2026.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akishiriki Ibada ya kumuaga na kumuombea Askofu wa Jimbo Katoliki Kondoa, marehemu Askofu Bernadin Francis Mfumbusa, iliyofanyika Katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Paulo wa Msalaba , Jimbo Kuu Katoliki Dodoma, leo tarehe 21 Aprili 2026.






Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akitoa salamu za rambirambi mara baada ya Ibada ya kumuaga na kumuombea Askofu wa Jimbo Katoliki Kondoa, marehemu Askofu Bernadin Francis Mfumbusa, iliyofanyika Katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Paulo wa Msalaba , Jimbo Kuu Katoliki Dodoma, leo tarehe 21 Aprili 2026.

MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amesema Taifa litaukumbuka mchango mkubwa aliyoutoa marehemu Askofu Bernadin Mfumbusa, enzi za uhai wake ikiwemo kuwa kiungo muhimu wa kuunganisha Kanisa Katoliki na Madhehebu mbalimbali pamoja na Dini zingine.

Makamu wa Rais amesema hayo mara baada ya kushiriki Ibada ya kumuaga na kumuombea Askofu wa Jimbo Katoliki Kondoa, marehemu Askofu Bernadin Francis Mfumbusa, iliyofanyika Katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Paulo wa Msalaba, Jimbo Kuu Katoliki Dodoma.

Amesema Marehemu Askofu Mfumbusa alijitolea katika kuunganisha dini na madhehebu ili zifanye kazi kwa kuheshimiana, kushirikiana na kupendana. Ameongeza kwamba Taifa litakumbuka mchango wake katika kuhamasisha elimu pamoja na kufanya kazi kubwa ya kuhamasisha na kusimamia ujenzi na uendelezaji wa huduma za Afya katika Wilaya ya Kondoa na Taifa kwa ujumla.

Makamu wa Rais amesema Marehemu Askofu Mfumbusa ametoa mchango katika sekta ya Mawasiliano na Habari akiwa mbobezi na mwalimu katika fani hiyo. Amesema Marehemu Mfumbusa atakumbukwa kwa kutimiza wajibu wake kwa binadamu kwa kutambua Maisha tunayoishi leo, na kutimiza wajibu wake kwa Mungu kwa kutuongoza katika njia ya uzima wa milele.

Aidha Makamu wa Rais amewasilisha salamu za pole za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, alizotoa kwa Kanisa, Waumini na Familia na kuiombea familia nguvu na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu.

Makamu wa Rais amewashukuru Viongozi wa Kanisa Katoliki kwa malezi ya marehemu Askofu Mfumbusa ambayo yalimfanya kuwa mtume wa Taifa zima.

Ibada hiyo, imeongozwa na Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki Dodoma Mhashamu Wilbroad Kibozi na kuhudhuriwa na Maaskofu mbalimbali, Mapadre, Watawa, Viongozi mbalimbali wa Serikali na Wananchi.

Imetolewa na
Ofisi ya Makamu wa Rais
21 Aprili 2026
Dodoma.



Na Mwamvua Mwinyi, Kibaha Aprili 21, 2026
KIONGOZI wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2026, Wazo Mwang’onda, ameweka jiwe la msingi katika kiwanda cha Doweicare Technology Ltd kilichopo Kata ya Misugusugu, Manispaa ya Kibaha, huku akiipongeza Serikali kwa kuweka mazingira rafiki kwa wawekezaji.

Kiwanda hicho kinajishughulisha na utengenezaji na usambazaji wa bidhaa za softcare kwa matumizi ya usafi, ikiwemo nepi za watoto na taulo za kike, kikiwa kimewekeza dola za Marekani milioni 16, sawa na takribani shilingi bilioni 40.

Akikagua na kuweka jiwe la msingi katika kiwanda hicho Aprili 21, 2026, Mwang’onda aligawa taulo za kike 6,000 kwa wanafunzi 1,000, zitakazowatosheleza kwa muda wa miezi sita.

Aidha, aliipongeza Manispaa ya Kibaha pamoja na Mkuu wa Wilaya hiyo kwa kuendelea kumpa ushirikiano Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kusimamia na kuimarisha sekta za uwekezaji na viwanda.

Awali, akipokea Mwenge wa Uhuru katika viwanja vya Shule ya Msingi Visiga, Kata ya Visiga, Manispaa ya Kibaha, Mkurugenzi wa Manispaa hiyo, Dkt. Rogers Shemwelekwa, alisema miradi nane yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 41.1 imezinduliwa, kukaguliwa na kuwekwa mawe ya msingi.

Miradi hiyo ni ujenzi wa barabara ya Kongowe–Forest, ujenzi wa vyumba vya madarasa katika Shule ya Sekondari Picha ya Ndege, na huduma za afya katika Zahanati ya Kilimahewa yenye thamani ya shilingi milioni 284.6.

Miradi mingine ni kisima kirefu cha maji safi katika Shule ya Msingi Tangini, mradi wa Kibaha Shopping Mall pamoja na mradi wa CJ-Chalya Plumbing Services unaohusisha shughuli za kikundi katika utengenezaji na uuzaji wa mabomba ya maji.

Mwenge wa Uhuru upo katika siku ya nne tangu kupokelewa mkoani Pwani Aprili 18, 2026, na unatarajiwa kupokelewa wilayani Mafia Aprili 22, 2026.




Na Mwandishi Wetu

Jumba la sanaa la Rangi Gallery la jijini Dar es Salaam limeandika historia baada ya kuwa taasisi ya kwanza kutoka Tanzania kushiriki katika maonesho ya kimataifa ya sanaa ya Art OnO 2026 yaliyofanyika jijini Seoul, Korea Kusini.

Maonesho hayo yaliyofanyika kuanzia Aprili 2 hadi 5 mwaka huu katika kituo cha maonesho cha SETEC, yameelezwa kuwa miongoni mwa majukwaa makubwa na yenye hadhi ya juu barani Asia yanayowakutanisha wadau wa sanaa kutoka mataifa mbalimbali duniani.

Kupitia ushiriki huo, Rangi Gallery ilisimama sambamba na majumba makubwa ya sanaa kutoka nchi 12 zikiwemo Japan, Ujerumani, Uswisi na mataifa mengine, hatua iliyotajwa kuiweka Tanzania katika ramani ya sanaa ya kisasa duniani.

Katika maonesho hayo, Rangi Gallery iliwasilisha kazi za wasanii wanne wanawake kutoka Tanzania ambao ni Theresia Venance, Tulsi Patel, Valerie Asiimwe Amani na Turakella Editha Gyindo.

Kazi za wasanii hao zilionesha upekee wa sanaa ya kisasa ya Kitanzania, zikigusa masuala ya utambulisho, mila, mabadiliko ya kijamii, uzoefu wa mwanamke pamoja na uhusiano wa binadamu na mazingira.

Mwanzilishi na Mkurugenzi Mtendaji wa Rangi Gallery, Lorna Mashiba Albou, alisema ushiriki huo ni ushahidi kuwa sanaa ya Tanzania ina uwezo mkubwa wa kushindana kimataifa.

“Wasanii wetu wameiwakilisha vyema Tanzania katika jukwaa hili la kimataifa. Hii inaonesha vipaji vya Kitanzania vinaweza kufika mbali vikipewa nafasi sahihi,” alisema Lorna.
Aliongeza kuwa licha ya wasanii wote waliowasilishwa kuwa wanawake, jambo hilo halikupangwa mahsusi bali lilitokana na ubora wa kazi zao.

Ushiriki wa Rangi Gallery pia umepewa uzito wa kidiplomasia baada ya Balozi wa Tanzania nchini Korea Kusini, Togolani Edriss Mavura, kuhudhuria maonesho hayo na kushuhudia kazi zilizooneshwa.

Wadau wa sanaa wameeleza kuwa hatua hiyo ni mwanzo wa safari kubwa kwa Tanzania katika soko la kimataifa la sanaa, huku baadhi ya wasanii walioshiriki wakitarajiwa kuiwakilisha nchi katika maonesho makubwa ya Venice Biennale 2026 nchini Italia.

Rangi Gallery ilianzishwa jijini Dar es Salaam na Lorna Mashiba Albou, ambaye awali alikuwa mwanasheria kabla ya kuhamia katika sekta ya uchumi wa ubunifu.

Mbali na kuonesha kazi za wasanii wa ndani, jumba hilo linaendesha programu ya Rangi Nyumbani Residency, inayolenga kuwaunganisha wasanii wa Tanzania na mitandao ya kimataifa.

Wachambuzi wanasema Tanzania imekuwa na vipaji vingi vya sanaa kwa miaka mingi, lakini changamoto kubwa imekuwa ukosefu wa majukwaa ya kuvitangaza. Kupitia juhudi za taasisi kama Rangi Gallery, sasa mlango wa dunia umeanza kufunguka kwa wasanii wa Kitanzania.

 

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia mafuta na gesi asilia, Dkt. James Mataragio,akisisitiza jambo kwa watumishi wa EWURA alipotembelea banda la EWURA  katika  maonesho ya Wiki ya Nishati 2026 yanayoendelea katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia mafuta na gesi asilia, Dkt. James Mataragio, amewaomba waheshimiwa wabunge na wadau mbalimbali kuendelea kutembelea maonesho ya Wiki ya Nishati 2026 yanayoendelea katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma, ili kupata elimu juu ya shughuli za kimkakati zinazotekelezwa na taasisi zilizo chini ya wizara hiyo pamoja na kubaini fursa za uwekezaji zinazopatikana.

Akiwa akiwa katika banda la Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), Dkt. Mataragio amesema mamlaka hiyo imeendelea kuwa nguzo muhimu katika kuhakikisha uwiano kati ya maslahi ya watoa huduma na watumiaji wa huduma zinazodhibitiwa, ikiwemo mafuta, gesi asilia na umeme.

“Tumeshuhudia jitihada kubwa zinazofanywa na EWURA katika kusimamia ubora wa huduma na bei stahiki, jambo ambalo linachangia kukuza uchumi na kulinda wananchi,” amesema Dkt. Mataragio.

Ameongeza kuwa uwepo wa EWURA katika maonesho hayo unatoa fursa kwa wananchi kupata elimu kuhusu haki na wajibu wao katika matumizi ya nishati, sambamba na kuelewa mifumo ya udhibiti inayolenga kuboresha huduma na fursa mbalimbali za uwekezaji.

Kwa upande wao, baadhi ya wabunge waliotembelea banda hilo pia waliipongeza EWURA kwa uwajibikaji wake, wakisema imekuwa mstari wa mbele kusikiliza na kushughulikia changamoto zinazowakabili wananchi katika sekta ya nishati pamoja na kuhakilisha upatikanaji wa huduma bora kwa wananchi.

Wiki ya Nishati 2026 imewakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya nishati, zikiwemo taasisi zote zilizo chini ya Wizara ya Nishati kwa lengo la kuonesha maendeleo na fursa zilizopo katika sekta hiyo muhimu kwa ustawi wa uchumi wa taifa.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia mafuta na gesi asilia, Dkt. James Mataragio,akipata maelezo kutoka kwa Kaimu Meneja wa Mawasiliano na Uhusiano wa EWURA, Bw.Wilfred Mwakalosi,alipotembelea banda la EWURA  katika  maonesho ya Wiki ya Nishati 2026 yanayoendelea katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia mafuta na gesi asilia, Dkt. James Mataragio,akipata maelezo kutoka kwa Kaimu Meneja wa Mawasiliano na Uhusiano wa EWURA, Bw.Wilfred Mwakalosi,alipotembelea banda la EWURA  katika  maonesho ya Wiki ya Nishati 2026 yanayoendelea katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia mafuta na gesi asilia, Dkt. James Mataragio,akisisitiza jambo kwa watumishi wa EWURA alipotembelea banda la EWURA  katika  maonesho ya Wiki ya Nishati 2026 yanayoendelea katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi, Dkt. James Mataragio akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kutembelea Banda la EWURA kwenye Maonesho ya Wiki ya Nishati 2026 yanayoendelea katika Viwanja vya Bunge Jijini Dodoma

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi, Dkt. James Mataragio akipokea zawadi kutoka kwa Kaimu Meneja wa Mawasiliano na Uhusiano wa EWURA, Bw.Wilfred Mwakalosi, mara baada ya kutembelea Banda la EWURA kwenye Maonesho ya Wiki ya Nishati 2026 yanayoendelea katika Viwanja vya Bunge Jijini Dodoma

Wabunge mbalimbali wakipata elimu walipotembelea banda la EWURA  katika  maonesho ya Wiki ya Nishati 2026 yanayoendelea katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia mafuta na gesi asilia, Dkt. James Mataragio,akizungumza mara baada ya kutembelea mabanda ya taasisi zilizo chini ya Wizara ya Nishati  katika  maonesho ya Wiki ya Nishati 2026 yanayoendelea katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma.


Top News