Na Mwandishi Wetu, Kigoma
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), Mohamed Salum, amesema mabaharia wana mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi wa taifa kutokana na nafasi yao muhimu katika usafirishaji wa bidhaa zinazoingia na kutoka nchini.
Salum aliyasema hayo wakati akifungua Warsha kuelekea kilele cha Maadhomisho cha Siku ya 16 ya Mabaharia Duniani yanayofanyika mkoani Kigoma, ambapo alieleza kuwa takribani asilimia 80 ya bidhaa zinazoingia nchini husafirishwa kwa njia ya maji na kufikishwa kwa watumiaji kupitia juhudi za mabaharia.
Alisema mchango wa mabaharia hauishii kwenye usafirishaji wa bidhaa pekee, bali pia una athari kubwa katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa kuhakikisha mnyororo wa biashara unaendelea kufanya kazi kwa ufanisi.
“Mabaharia ni nguzo muhimu ya uzalishaji na maendeleo ya uchumi. Bila wao, shughuli nyingi za biashara na usafirishaji zingekwama,” alisema Salum.
Aliongeza kuwa TASAC itaendelea kusimamia na kuratibu sekta ya mabaharia kwa kuhakikisha viwango vya kitaaluma na usalama vinazingatiwa ili mabaharia wa Tanzania waendelee kuwa na ushindani katika soko la ajira duniani.
Akizungumzia changamoto zinazowakabili mabaharia, Salum alisema migogoro inayoendelea katika baadhi ya maeneo duniani, ikiwemo mvutano kati ya Iran na Israel unaohusisha njia muhimu za usafiri wa majini, imeongeza hatari kwa mabaharia wanaotekeleza majukumu yao katika maeneo hayo.
Alibainisha kuwa Tanzania tayari imepoteza mmoja wa mabaharia wake kutokana na changamoto zinazotokana na mazingira ya migogoro, jambo linalosisitiza umuhimu wa kuimarisha ulinzi na usalama wa wafanyakazi hao wanapokuwa kazini.
“Tunahitaji kuona juhudi zaidi za kimataifa katika kulinda mabaharia, kwa sababu wao ndiyo uti wa mgongo wa sekta ya usafirishaji wa majini duniani,” alisema.
Aidha, alisisitiza umuhimu wa mabaharia kushiriki kikamilifu katika kulinda mazingira ya bahari na maziwa, akieleza kuwa mfumo wa ikolojia wa maeneo hayo una umuhimu mkubwa kwa maisha ya viumbe hai na ustawi wa jamii zinazotegemea rasilimali za maji.
Salum pia alitaja Ziwa Tanganyika kuwa moja ya nyenzo muhimu za uchumi wa Tanzania kutokana na kuunganisha Tanzania na nchi nne jirani, hivyo kutoa fursa kubwa za biashara, usafiri na maendeleo kwa wananchi wa ukanda huo.
Aliwahimiza mabaharia kuendelea kufanya kazi kwa weledi na uzalendo huku akiihakikishia jamii ya mabaharia kuwa Serikali kupitia TASAC itaendelea kuthamini mchango wao, kuimarisha usalama wao na kuboresha mazingira ya kazi ili sekta hiyo iendelee kuwa kichocheo muhimu cha ukuaji wa uchumi wa taifa.
Mkurugenzi Mkuu wa TASAC Mohamed Salum akizungumza wakati akifungua Warsha ya Mabaharia kuelekea Kilele cha Maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani Mjini KigomaMkuu wa Chuo cha DMI Profesa Tumaini Gurumo akizungumza katika Warsha ya Mabaharia katika Maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani mkoani Kigoma.
Matukio katika picha katika Warsha ya Mabaharia mkoani Kigoma










.jpeg)




















.jpeg)








.jpeg)








