Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Kibamba, Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki, amefanya ziara ya kukagua na kutembelea miradi mbalimbali ya maendeleo inayoendelea katika Kata ya Saranga, ikiwa ni sehemu ya jitihada zake za kuhakikisha wananchi wanapata miundombinu bora na huduma zinazokidhi mahitaji yao ya kila siku.

Katika ziara hiyo, Mheshimiwa Kairuki alitembelea Barabara ya King’ongo, kipande cha urefu wa mita 200 kilichopo karibu na Ofisi ya TRA Kimara Mwisho, ambacho kinajengwa kwa kiwango cha zege.

Barabara hiyo inatarajiwa kuboresha usafiri na kuongeza usalama kwa wananchi wanaoitumia.

Aidha, Mbunge huyo alikagua pia Barabara ya Suka Golani yenye urefu wa kilometa 1.5, ambayo imechongwa kwa kujazwa kifusi na kushindiliwa, hatua inayolenga kurahisisha upitishaji wa magari pamoja na kuboresha shughuli za kijamii na kiuchumi kwa wakazi wa eneo hilo.

Katika ziara hiyo, Mheshimiwa Kairuki alipata fursa ya kuwasikiliza wananchi wa Kata ya Saranga waliowasilisha kero zao mbalimbali, hususan changamoto ya uhaba wa vivuko salama katika baadhi ya maeneo.

Mbunge huyo alisifu moyo wa ushirikiano uliooneshwa na wananchi waliokwisha anza kuchangia ujenzi wa baadhi ya vivuko, na kuahidi kutoa sapoti ili kuhakikisha changamoto hiyo inapatiwa ufumbuzi wa kudumu.

Vilevile, Mheshimiwa Mbunge alitembelea Mtaa wa Upendo, ambako wananchi walieleza hamu yao ya kuona ujenzi wa shule katika mtaa huo ili kusogeza huduma ya elimu karibu na watoto wao.

Ziara hiyo imeacha faraja na matumaini mapya kwa wananchi wa Kata ya Saranga, ambao wameonesha imani yao kwa uongozi wa Mbunge wao na kuahidi kuendelea kushirikiana katika kusukuma mbele gurudumu la maendeleo.





Katika jitihada za kuboresha sekta ya elimu nchini Tanzania, ADEM na Taasisi ya Project Zawadi wameingia makubaliano ya ushirikiano utakaowezesha kuendesha mafunzo ya muda mfupi kuhusu uongozi, usimamizi na uendeshaji wa elimu kwa viongozi wa Mkoani Mara. 

Ushirikiano huu unalenga kuwajengea uwezo viongozi wanaosimamia sekta ya elimu kuanzia ngazi ya shule hadi Mkoa

Akizungumza katika hafla hiyo ya utiaji saini hati ya makubaliano ya ushirikiano (MoU) kati ya ADEM na Project Zawadi, Mtendaji Mkuu Dkt. Maulid J. Maulid amesema lengo la Makubaliano hayo ni kuweka msingi wa ushirikiano baina ya Taasisi hizo mbili kwa ajili ya kuandaa na kutekeleza programu za mafunzo ya muda muda mfupi kuhusu uongozi na usimamizi wa elimu nchini.

“Ili taasisi zenye majukumu yanayofanana ziweze kuboresha utendaji wake ni muhimu kuepuka kufanya kazi kwa kujitenga, zinahitaji kujenga ushirikiano na uhusiano katika kuimarisha utekelezaji wa majukumu yao kwa ufanisi na kuleta tija na manufaa kwa taasisi husika na Serikali kwa ujumla. Kwa kuwa rasilimali za Serikali katika eneo la utoaji wa mafunzo kwa viongozi wa elimu bado hazitoshelezi hivyo ni vyema taasisi zisizo za Serikali kuunga mkono juhudi za Serikali kwa kuhakikisha zinasaidia kuimarisha uongozi na usimamizi wa elimu kwa kuwezesha mafunzo hayo kama walivyofanya taasisi ya Project Zawadi katika mkoa wa Mara ambapo katika kutekeleza hilo wameamua kushirikiana na ADEM”.

Nae Mkurugenzi Mkaazi Project Zawadi nchini Bw. Raymond Gilbert akizungumza katika hafla hiyo amesema kuwa Taasisi yake inaamini katika ujuzi, utaalamu na uwezo wa ADEM katika kuleta mabadiliko chanya kwenye eneo la uongozi na usimamizi wa elimu kwa kuwajengea uwezo viongozi mbalimbali wa elimu nchini ili kuimarisha usimamizi wa shughuli za ufundishaji na ujifunzaji.

Hafla hii ya utiaji saini imefanyika leo Februari 2, 2026 ADEM Bagamoyo ambapo ushirikiano huu unatarajiwa kuimarisha utendaji na kuongeza ufanisi katika sekta ya elimu nchini ukihusisha kuwajengea uwezo viongozi wa elimu Mkoani Mara.



Picha namba 01. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Al Maktoum (DWC) Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), tarehe 2 Februari, 2026. Rais Mhe. Dkt. Samia atashiriki kwenye Mkutano wa Dunia wa Serikali (World Governments Summit – WGS) 2026 pamoja na kushiriki Jukwaa la Kimataifa wa Uwekezaji Afrika (GAIS).

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Waziri wa Sheria wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) Abdullah bin Sultan bin Awad al Nuaimi mara baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Al Maktoum (DWC) Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), tarehe 2 Februari, 2026. Rais Mhe. Dkt. Samia atashiriki kwenye Mkutano wa Dunia wa Serikali (World Governments Summit – WGS) 2026 pamoja na kushiriki Jukwaa la Kimataifa wa Uwekezaji Afrika (GAIS).
 

 

 

Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese,akizungumza wakati wa maadhimisho ya Siku ya Sheria yaliyofanyika katika Mahakama ya Wilaya ya Handeni leo Februari 2,2026.

Na Augusta Njoji

Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, ametoa rai kwa Mahakama ya Wilaya ya Handeni kutoa kipaumbele katika usikilizwaji wa mashauri yanayohusu ardhi ili yahitimishwe kwa wakati na kuchochea maendeleo ya wananchi.

Akizungumza wakati wa maadhimisho ya Siku ya Sheria yaliyofanyika katika Mahakama ya Wilaya ya Handeni, Mhe. Nyamwese amesema migogoro ya ardhi imekuwa ikichukua muda mrefu kusikilizwa pindi inapofikishwa mahakamani, hali inayosababisha kucheleweshwa kwa utekelezaji wa shughuli za maendeleo.

Amesema ardhi ni rasilimali muhimu katika Wilaya ya Handeni, lakini imeendelea kukumbwa na migogoro mingi, ambayo baadhi yake haina tija kwa maendeleo ya jamii.

Amesisitiza kuwa haki inapocheleweshwa, maendeleo nayo hucheleweshwa, hususan pale wananchi wanapokusudia kutumia ardhi kwa uwekezaji au shughuli za uzalishaji.

“Sisi kama Wilaya tumekuwa na migogoro ya ardhi, lakini inapofika mahakamani mashauri haya huchukua muda mrefu kusikilizwa. Hali hii inawaathiri wananchi na kudumaza maendeleo kwa ujumla,” amesema Mhe. Nyamwese.

Aidha, amepongeza hatua zilizochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuboresha utendaji wa Mahakama, ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya mahakama karibu na wananchi pamoja na matumizi ya teknolojia, hatua zinazoongeza imani ya wananchi katika mfumo wa utoaji haki.

Kwa upande wake, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Wilaya ya Handeni, Joseph Waruku, amesema Mahakama imeendelea kusogeza huduma karibu na wananchi kwa kuanzisha Mahakama za Mwanzo 12 mwaka 2025 katika maeneo yenye msongamano wa mashauri, ikiwemo Mahakama ya Mwanzo Msomera.

Naye, Mwakilishi wa Mwanasheria wa Halmashauri ya Mji Handeni, Regina Pangah, amesema Mahakama zina mchango mkubwa katika ustawi wa jamii na ukuaji wa uchumi kwa kuhakikisha haki inapatikana kwa wakati, huku akiahidi kuendeleza ushirikiano katika kutoa elimu ya sheria kwa wananchi.

Dar es Salaam 02 Februari, 2026

Jumuiya ya Wazazi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Dar es Salaam leo tarehe 02 Februari, 2026, imeungana na wanaCCM na wananchi kwa ujumla kuadhimisha kilele cha miaka 49 ya kuzaliwa kwa Chama Cha Mapinduzi, kwa kufanya shughuli mbalimbali za kijamii katika Wilaya ya Temeke.

Katika maadhimisho hayo ya kimkoa, Jumuiya ya Wazazi Mkoa wa DSM ilitembelea Hospitali ya Round Table Mbagala, wodi ya wazazi, na kutoa msaada wa vifaa vya kujifungulia (delivery kits) kwa akina mama wajawazito 22.

Aidha, msaada huo uliambatana na ugawaji wa pampers, sabuni pamoja na maji ya kunywa, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono afya ya mama na mtoto.

Kadhalika, Jumuiya ilitembelea Kituo cha Hiari Orphanage Center, ambapo ilikabidhi mahitaji maalum kwa ajili ya kuwasaidia watoto wanaolelewa katika kituo hicho, ikiwa ni ishara ya mshikamano na upendo kwa makundi yenye uhitaji maalum.

Kwa sasa, viongozi na wajumbe wa Jumuiya ya Wazazi Mkoa wa Dar es Salaam wamekutana katika ukumbi wa Ikweta Grill – Mtoni kwa ajili ya kikao cha ndani, ambapo pia kutatolewa viti mwendo (wheelchairs) vinne kwa watoto wenye uhitaji maalum.

Jumuiya ya Wazazi inaendelea kusisitiza dhamira yake ya kushiriki kikamilifu katika kujenga jamii bora, yenye mshikamano na maendeleo kwa maslahi mapana ya Taifa.
Happy 49th Birthday CCM!

Wazazi tupo mtaani kujenga jamii bora kwa maslahi ya Taifa.
Imetolewa na:

Jumuiya ya Wazazi CCM Mkoa wa Dar es Salaam.














Na Said Mwishehe


KITENDO cha kushambuliwa kwa Mwenyekiti wa Klabu ya Simba Multaza Ally Mangungu jana baada ya kumalizika kwa mechi kati ya SIMBA na ESPERANCE kimetuudhi mashabiki wa soka Tanzania naamini hata Duniani.

Sio kitendo cha kiungwana hata kidogo kilichofanywa na baadhi ya mashabiki wa Simba ambao kupitia video mjongeo(video fupi)wameonekana wakimshambulia Mangungu na mmoja wa mashabiki akionekana kabisa akimpiga ngumi

Ni mambo ya hovyo kabisa, ni mambo ya kijinga na ni ushamba uliopiilitiza. Ni ushabiki wa kizamani na wengine tulishasahau matukio ya Viongozi wa soka hapa Tanzania kushambuliwa.

Tujiulize kwa akili ya kawaida kosa la Mangungu ni lipi ?Ile sare ya 2-2 ambayo imepatikana jana Mangungu anahusika vipi?

Alikuwepo ndani ya Uwanja akicheza? Yeye ndiye aliyetoa ile pası ya hovyo iliyosababisha ESPERANCE wapate goli la kwanza kabla ya kufunga goli la pili na kufanya mchezo kumaliza kwa sare ya 2-2.

Najaribu kujiuliza waliomshambulia Mangungu wanajua majukumu yake pale SIMBA? Wanajua mipaka yake ya kutekeleza majukumu yake inaanzia wapi na kuishia wapi?

Unamshambuliaje kiongozi ambaye yeye sio kocha,hapangi timu wala hakai benchi la ufundi? Sawa Mangungu yuko pale SIMBA kwa nafasi ya Mwenyekiti hebu tujiulize yuko peke yake?

Hakuna viongozi wengine pale SIMBA? Kwanini kila siku yeye? SIMBA ikifanya vizuri Mangungu wala hakuna anayemtaja hata kumpongeza lakini timu ikifungwa basi Mangungu .

Wana Simba na hasa mashabiki OYA OYA acheni mambo ya kijinga.Simba ni ya Wana Simba wote. Kumekuwa na tabia siku hizi kwa baadhi ya mashabiki wanajifanya wenyewe ndio wanaumizwa sana na SIMBA kufanya vibaya, hovyo kabisa.

Timu ikishinda wako kimya ,ikifungwa wanakimbilia mitandaoni kutukana viongozi na wachezaji. Ni mashabiki wa hovyo sana.

Ni mashabiki wasiojitambua.Tunafahamu Simba ina wanachama, mashabiki na wapenzi ambao wanaipenda timu yao, wanawapenda viongozi wao na wanawapenda wachezaji.

Wao wapo na timu bila kujali nyakati wanazopitia. Ni SIMBA hii na Mangungu akiwa Mwenyekiti imefanya makubwa katika soka la Tanzania ,soka la Afrika Mashariki na Afrika kwa ujumla.

Nani ambaye hajui ukubwa wa Simba Afrika? Iko nafasi ya tano kwa ubora.Katika mafanikio hayo ya Simba huwezi kuliacha jina la Mangungu kwani kama kiongozi ana mchango wake katika mafanikio hayo.

Simba imekuwa bingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara Mara nne mfululizo na sio miaka mingi iliyopita,sasa kwanini Wana Simba hasa ninyi mashabiki uchwara mnajisahaulisha.

Mangungu amepatikana kupitia uchaguzi mkuu wa Simba kama humtaki wakati ukifika kachukue fomu ugombee au kamchukulie fomu huyo unayemuona anafaa kuwa Mwenyekiti wa Simba.

Haya mambo ya kumshambulia hakuna anayefurahishwa. Niliombe Jeshi la Polisi kuchukua hatua dhidi ya wale wote ambao wameonekana wakimshambulia Mangungu.

Kupitia video zinazosambaa mtandaoni wale wote wakamatwe na wachukukuliwe hatua. Kuna haja ya kukomesha tabia hii kabla haijakomaa na kuharibu soka la Tanzania, kukatisha tamaa viongozi.

Ni wakati wa wadau wa soka kukemea tabia hii.Katika Ulimwengu wa soka wanaamini katika soka ni burudani,soka ni furaha na kubwa zaidi soka inaongozwa na Fair Play.

Mwenyekiti Mangungu pole, tunakuombea kwa Muumba wa mbingu na ardhi aendelee kukupa afya na uzima.

Tunakuombea kwa Mungu aendelee kukupa hekima ,busara na maarifa katika kuendelea kutekeleza majukumu yako ndani ya Klabu ya Simba.

Wadau wa soka nchini tunaheshimu na kutambua mchango wako.Ila nikunong’oneze kuna baadhi ya Wana Simba wenzako ndio wanaeneza propaganda chafu ili kukuchafua .

Kuwa makini kwani kwa ile video ya jana unaona kabisa ni kama kuna watu nyuma yao waliotengeneza tukio lile ili ushambuliwe,unyanyasike uwanjani.Pole Mangungu but tunajua wewe ni kiongozi imara na hivyo utabaki kuwa imara.


Simu 0713833822.




Na Jackline Minja – WJJWM Dodoma.

Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi amesema Serikali imejipanga kuhakikisha wanawake wajasiriamali wanashiriki kikamilifu katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050, hususan katika nguzo za uchumi imara, jumuishi na shindani pamoja na maendeleo ya jamii.

Ameyasema hayo tarehe 02 Februari 2026 Bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Janeth Elias Mahawanga, ambalo liliuliza kuwa “Je Serikali imejipangaje kuhakikisha wanawake wajasiliamali wanashiriki moja kwa moja kwenye utekelezaji wa dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050”?

Akijibu swali hilo Mhe. Mahundi amesema Serikali imeweka mikakati mbalimbali itakayowawezesha wanawake wajasiriamali kushiriki moja kwa moja katika maendeleo ya taifa kupitia shughuli za kiuchumi.

Mhe. Mahundi amesema mikakati hiyo inalenga kupunguza vikwazo vinavyowakabili wanawake katika upatikanaji wa mitaji na masoko ili kuongeza uzalishaji na ushindani wa bidhaa na huduma zao.

Mhe. Mahundi ameongeza kuwa Serikali inaendelea kubuni na kutekeleza jitihada mahsusi za kuwawezesha wanawake na wanaume kunufaika na fursa za kiuchumi, ikiwemo utekelezaji wa majukwaa ya uwezeshaji wanawake kiuchumi pamoja na kuwapatia mafunzo ya ujasiriamali, matumizi ya teknolojia na viwanda vidogo na vya kati.

"Hatua hizo zitasaidia biashara za wanawake kukua, kuongeza ajira na kuchangia kikamilifu katika uchumi wa taifa kuelekea kufikiwa kwa malengo ya Dira ya Maendeleo 2050." amesema Mhe. Mahundi.




Na WAF, Dar es Salaam

Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amesema wahariri wa vyombo vya habari wana jukumu muhimu la kubadilisha hofu ya wananchi kuwa uelewa sahihi kuhusu Bima ya Afya kwa Wote, ili waweze kunufaika kikamilifu na huduma za afya.

Amesema hayo leo, Februari 2, 2026, wakati akizungumza katika kikao kazi na wahariri kilichofanyika Ukumbi wa Karimjee, Dar es Salaam.

“Hofu huzaa hasira, na hasira huzaa mgawanyiko. Sauti zenu ni dira, na kalamu zenu ni mwanga utakao waongoza wananchi kesho,” amesema Waziri Mchengerwa.

Ameongeza kuwa wahariri wanapaswa kutumia nafasi yao kuwaelimisha wananchi kwa usahihi kuhusu mfumo wa Bima ya Afya kwa Wote, ili kuondoa upotoshaji na kuongeza uelewa wa huduma zitakazotolewa.

Aidha Waziri Mchengerwa amesema kuwa Serikali imejipanga vyema ili kutekeleza mpango wa Bima ya Afya kwa wote husuasan ni eneo la makundi maalum pamoja na matibabu ya magonjwa sugu ili mwananchi aweze kufurahia huduma za afya nchini.

"Mhe. Rais atakapokwenda kuzindua Bima ya Afya kwa wote atazindua pia mpango wa matibabu ya wale wasiojiweza (wazee na makundi maalum) hasa kwenye matibabu ya magonjwa sugu, sisi kama wizara tumeshajipa na kujiandaa katika utekelezaji," amesema Waziri Mchengerwa








📌 Shilingi bilioni 43.9 kusambaza umeme kwenye vitongoji 379

📌 Kampuni ya Giza Cable kuanza kazi ya kusambaza umeme vitongoji vya mkoa wa Dodoma

📌 Wananchi zaidi ya 12,000 kufikishiwa huduma hiyo


Mkuu wa mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule ametoa wito kwa Wananchi wa vitongoji vitakavyonufaika na Mradi wa Kusambaza Umeme katika vitongoji 379 kujiandaa kwa kutandaza nyaya majumbani (Wiring) mapema ili kuunganishwa na huduma hiyo mara Mradi utakapokamilika.

Akizungumza wakati wa hafla ya kumtambulisha mkandarasi huyo (Kampuni ya Giza Cable Industries S.A.E) kutoka Misri ambaye anatekeleza Mradi wa kusambaza umeme katika vitongoji 379 vya mkoa wa Dodoma; Mhe. Senyamule alisema ni muhimu Wananchi kuwekeza mapema katika miundombinu ya ndani ya majengo yao ili kuepuka kuchelewa kupata huduma hiyo.

Mkuu huyo wa mkoa alitoa rai kwa mkandarasi huyo kuhakikisha kazi hiyo ya kusambaza umeme katika vitongoji 379 inakamilika sawa sawa na mkataba au ikiwezekana kabla ya muda uliopangwa.

Aidha, Mkuu wa mkoa Senyamule alionya vikali dhidi ya vishoka; wanaopita kwa Wananchi wa maeneo mbalimba ya mkoa huo akisema kuwa Serikali ya mkoa imejipanga ili kuhakikisha jambo hilo halitokei tena na kutoa wito kwa Wananchi wanawatumia mafundi wenye ujuzi na wanaotambulika kisheria katika kufanya ‘wiring’ ya umeme kwenye nyumba zao.

Kwa upande wake; Mhandisi Msimamizi wa Miradi ya REA Kanda ya Kati, Aneth Malingumu alisema hafla hiyo imelenga kumtambulisha rasmi mkandarasi ili aanze kazi ya kusambaza umeme katika vitongoji vya mkoa wa Dodoma ambapo Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 43.9 kwa ajili ya Mradi huo wa kusambaza umeme kwenye vitongoji 379 katika wilaya ya Chamwino; Kongwa; Mpwapwa; Kondoa na Chemba.

Alisema mradi huo utawezesha Wateja wa awali (Wananchi 12,256) kupata huduma ya umeme na kuongeza kuwa huduma ya umeme ikitumiwa vizuri, itasaidia kuinua uchumi wao pamoja na kuboresha utoaji wa huduma za kijamii ikiwemo afya na elimu.

Mhandisi Malingumu aliwahimiza Wananchi kuhakikisha wanafanya ‘wiring’ ya ndani ya nyumba mapema ili wawe tayari kuunganishwa na umeme mara miundombinu itakapokamilika na aliongeza kuwa REA itaendelea kushirikiana na mkandarasi ili kutatua changamoto katika maeneo ya kazi na kumlipa kwa wakati ili mradi ukamilike ndani ya muda wa mkataba wa miaka mitatu.

Naye Meneja wa TANESCO Mkoa wa Dodoma, Mhandisi, Donasia Shamba, alisema TANESCO ambaye ndiye Mtaalam Elekezi (Consultant) watahakikisha vifaa pamoja ujenzi wa Mradi huo unazingatia ubora unahitajika ili malengo ya Serikali kupitia REA yafanikiwe.

Kwa upande wake, Mhandisi, Almas Msuya; Mwakilishi wa kampuni ya Giza Cable alisema kampuni hiyo iko tayari kutekeleza maagizo yote yaliyotolewa na Serikali ili kuhakikisha mradi wa kusambaza umeme katika vitongoji 379 unakamilika kwa wakati kulingana na masharti ya mkataba.







-Lengo ni kufikisha umeme kwenye vitongoji vyote nchini ifikapo 2030

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) unaendelea kutekeleza miradi ya kusambaza umeme vitongojini kwa lengo la kuhakikisha ifikapo Mwaka 2030 vitongoji vyote viwe vimefikishiwa umeme.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa REA, Meneja wa Usimamizi wa Miradi ya Kusambaza Umeme REA, Mha. Deogratius Nagu ameyasema hayo Mkoani Ruvuma Februari 1, 2026 wakati wa ziara ya kukagua miradi ya kusambaza umeme inayotekelezwa mkoani ili kujionea hali ya utekelezaji.

“Tupo katika Mkoa wa Ruvuma kwa lengo la kukagua miradi mbalimbali ya kusambaza umeme vitongojini inayotekelezwa na Wakala na leo hii tumefika hapa Wilayani Mbinga kukagua mradi wa kupeleka umeme vitongoji 148 ujulikanao kama Mradi wa Ujazilizi Fungu 2C (Densification 2C) unaohusisha Wilaya ya Songea, Mbinga na Nyasa,” amefafanua Mhandisi Nagu

Katika ziara hiyo, Mha. Nagu amemuelekeza Mkandarasi anayetekeleza mradi, kampuni ya MF Electrical Engineering Ltd kuhakikisha anaongeza kasi ya ujenzi wa mradi ili akamilishe usambazaji wa umeme katika vitongoji 60 vilivyosalia katika mradi huo.

“Huu mradi unahusisha usambazaji umeme katika vitongoji 148 ambapo vitongoji 88 tayari vimewashwa umeme na kubakiza vitongoji 60 ambavyo utekelezaji unaendelea; tumemuelekeza Mkandarasi kuhakikisha anakamilisha mapema kazi ya kusambaza umeme katika vitongoji alivyobakiza,” amesema Mha. Nagu.

Akizungumza kwa niaba ya Msimamizi wa Miradi ya REA Mkoa wa Ruvuma, Mhandisi Zakaria Ng’okorome amesema mradi unatekelezwa kwa gharama ya shilingi bilioni 18.294 na kwamba utanufaisha wateja wa awali wapatao 6,781.

Naye Msimamizi wa Mradi kutoka Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Mkoa wa Ruvuma, Mha. Ali Pandit alisema wamejipanga kikamilifu kuhalkikisha miradi inakamilika kwa wakati na kufikisha umeme kwa wananchi.

Kwa upande wake Msimamizi wa Mradi upande wa Mkandarasi, Mha. Musa David amesema wamepokea maelekezo na kuahidi kukamilisha mradi kwa wakati.






Top News