Kituo cha Zana za Kilimo na Teknolojia Vijijini (CAMARTEC) kimeanzisha mbinu mpya za mafunzo kwa wakulima kuhusu usindikaji wa mazao, ikiwemo mwani korosho na vyakula vingine, ili kuhakikisha wakulima wanapunguza hasara wanaposafirisha bidhaa zao sokoni, huku teknolojia hiyo ikiongeza muda wa kukaa kwa bidhaa bila kuharibika.

Vilevile, Katika kukabiliana na changamoto ya uhaba wa malisho inayowakabili wafugaji wengi nchini, kituo hicho kimebuni teknolojia ya kuchakata mabua ya mahindi na magunzi kwa ajili ya kutengeneza chakula cha mifugo ili kunusuru mifugo dhidi ya athari za ukame, ambao umekuwa ukisababisha hasara kubwa ya kiuchumi kwa wafugaji kutokana na vifo na kupungua kwa tija ya mifugo yao.

Hayo yamesemwa Januari 19, 2026 na Naibu Waziri Dennis Londo alipotembelea kituo hicho na kukiagiza kuongeza kasi ya ubunifu ili kumwondoa mkulima katika matumizi ya jembe la mkono na kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050.

Aidha, alisema pamoja na Mafanikio kilichonacho ni muhimu kwa kituo hicho kutafuta wabia katika halmashauri mbalimbali nchini ili kuhakikisha zana hizo zinazalishwa kwa wingi na kuwafikia wananchi vijijini na kuibadili sekta ya kilimo kuwa fursa ya kibiashara

Waziri Londo pia aliongeza kuwa ukosefu wa teknolojia rafiki unasababisha matumizi ya ardhi kubwa kuzalisha mazao machache, hivyo CAMARTEC inapaswa kuhakikisha teknolojia zao zinawafikia wakulima ili wajikwamue kiuchumi.

Awali, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa CAMARTEC, Mhandisi Godfrey Mwinama, alieleza kuwa kituo kimeanzisha mashamba darasa ili kuwawezesha wakulima kujifunza kwa vitendo matumizi ya zana bora kama mashine za kuchanjua mahindi, matrekta ya kisasa, na teknolojia za usindikaji zinazorahisisha kazi za shambani.

Aidha, CAMARTEC imeweka nguvu kubwa katika uzalishaji wa mitambo ya kubangua korosho kwa ajili ya wakulima wa mikoa ya Lindi, Mtwara, na maeneo mengine yanayozalisha zao hilo ili kuongeza thamani katika mnyororo wa zao la korosho na kuwasaidia wakulima kupata soko la uhakika na bei nzuri zaidi kuliko kuuza zao ghafi.

Naye Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Sera na Mipango, Audax Bahweitama, alihimiza kituo hicho kuhakikisha kuwa zana zote zinazobuniwa zinauzwa kwa bei nafuu na inayohimilika kwa mkulima mdogo. Alieleza kuwa upatikanaji wa zana hizo maeneo ya vijijini utachochea ukuaji wa uchumi wa taifa na kuongeza mapato ya serikali kupitia mnyororo wa thamani unaoanzia shambani hadi viwandani.







 

SHIRIKA la Uhandisi na Usanifu Mitambo Tanzania (TEMDO) limebuni, kusanifu na kutengeneza mtambo wa kuchakata zao la miwa ili kupata sukari kwa kiwango cha mjasiriamali wa kati, ikiwa ni jitihada za kupunguza uhaba wa sukari nchini pamoja na kuwaongezea wakulima wa miwa soko la uhakika.

Hayo yalisemwa Januari 19, 2026 na Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dennis Londo (Mb.), wakati wa Ziara yake TEMDO jijini Arusha ambapo amelishauri Shirika hilo kuzalisha mitambo hiyo ya Sukari pamoja na mitambo mingine katika kanda zote nchini kwa kushirikiana na taasisi mbalimbali za ndani ikiwemo TAMISEMI na nje ya nchi, ili kufikia Malengo yanayotarajiwa.

Aidha, aliiagiza TEMDO kuzalisha mitambo inayoendana na kasi ya teknolojia ili kuhakikisha teknolojia zinazozalishwa zinaingia sokoni na kutoa fursa zaidi za kiuchumi na kuondokana na umaskini kwa Wajasiliamali na Wananchi kwa ujumla.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya TEMDO, Kanali Mstaafu Joseph Simbakalia, alisema Shirika hilo linaendelea kuweka mikakati madhubuti ya mageuzi ya viwanda kwa kuzalisha mitambo itakayotatua changamoto za wakulima na kuwawezesha kupata masoko ya uhakika ili kuongeza uzalishaji viwandani na kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050.

Awali, Mkurugenzi Mkuu wa TEMDO, Profesa Frederick Kahimba alisema kuwa kukamilika kwa mradi huo kutasaidia kupunguza pengo la uzalishaji wa sukari nchini sambamba na kuongeza thamani ya zao la miwa kwa wakulima wadogo na wa kati ambapo hadi sasa Shirika hilo limepokea maombi sita kutoka kwa Wajasiliamali wa kati wanaotaka kufungiwa mitambo hiyo ya Sukari kutoka Dodoma, Same, Manyara, Busega, Kilosa na Morogoro.

Temdo inazalisha bidhaa zaidi ya 16 ikiwemo vifaa tiba vya hospitali kama majokofu ya kuhifadhia maiti, vichomea taka hatarishi, vitanda vya aina mbalimbali vinavyohitaji kufika soko la Zanzibar ili kuongeza pato la Taifa, kukuza uchumi na kupunguza uagizaji wa bidhaa hizo kutoka nje ya nchi. Alifafanua Kahimba.

Naye Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Sera na Mipango wa wizara hiyo, Audax Bahweitama akimwalikilisha Katibu Mkuu wa Wizara hiyo alisema Serikali improvises Sera na Sheria mbalimbali zinazohusu Maendeleo ya Viwanda ili kufikia uchumi jumuishi kupitia viwanda kwa kuzalisha bidhaa zenye ushindani na ubora sokoni, kama ilivyoainishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050. 

 
Serikali inaendelea na mkakati kuimarisha ushirikiano na sekta binafsi pamoja na wadau wa maendeleo katika suala la huduma ya maji safi na usafi wa mazingira kwa kuzingatia Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050.

Kaimu Katibu Mkuu , Wizara ya Maji Bwn. Henry Chisute amesema akifungua Warsha ya uhakiki na Kujenga Uwezo, iliyofanyika Mji wa Serikali, Mtumba jijini Dodoma.

Amesema Tanzania imepiga hatua nzuri katika eneo la upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama pamoja na usafi wa mazingira.

Amesema ongezeko la idadi ya watu, kasi ya miji kukua, na athari zinazoongezeka za mabadiliko ya tabianchi zinaendelea kuongeza shinikizo katika mifumo ya maji na usafi wa mazingira. Hivyo inalazimu kuendelea kuboresha na kuimarisha mbinu za kufikisha huduma kwa wananchi.

Ameainisha jitihada za serikali pekee hazitoshi kufikia ukubwa wa malengo hivyo ni muhimu sekta binafsi ishiriki kwa nguvu zaidi, kwa mpangilio mzuri na kwa ubunifu katika utoaji wa huduma, uwekezaji na uendelevu.

Ameongeza lengo la Serikali si kuhamisha jukumu kutoka taasisi za umma, bali ni kujenga mfumo imara zaidi ambapo wadau wa umma na binafsi wanajumuishwa katika kutoa huduma ya maji na usafi wa mazingira.

Warsha imehudhuriwa na wawakilishi kutoka Wizara, Idara na Taasisi za Serikali , Sekta binafsi na washirika wa maendeleo ikiwemo Benki ya Dunia, Benki ya Maendeleo ya Afrika, UNICEF, GIZ, AFD na KfW.






Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Ndugu Kenani Laban Kihongosi, amemuagiza Waziri wa Afya Mhe. Mohamedy Mchengerwa kuhakikisha gari la wagonjwa(Ambulance)linafika katika Hospitali ya Wilaya Singida Vijijini haraka iwezekanavyo.

Alitoa rai hiyo leo Jumatatu January 19 baada ya kukagua ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Singida Vijijini, iliyopo Ilongero, mradi unaogharimu Tsh. bilioni 3.7 katika siku ya pili ya ziara yake ya siku tano mkoani Singida.

Komredi Kihongosi alimpigia simu Waziri wa Afya Mhe. Mohamedy Mchengerwa na kuigiza wizara hiyo kuhakikisha gari hilo linafika kwa wakati.

Gari hili litarahisisha usafiri wa haraka kwa wagonjwa kutoka tarafa tatu zinazotegemea huduma kutoka hospitali hiyo, na hivyo kuondoa usumbufu mkubwa wa huduma ya afya kwa wakazi wa vijiji vilivyombali.














Chama Cha Mapinduzi kimetaka kumalizwa haraka kwa ujenzi wa Soko la Kimataifala Vitunguu katika Manispaa ya Singida.

Maelekezo hayo yametokewa leo tarehe 19 Januari 2026 na  Katibu wa NEC Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Kenani Kihongosi, alipofanya ziara ya kikazi kukagua maendeleo ya ujenzi wa Soko hilo.

“Chama Cha Mapinduzi kimetoa maelekezo kwa mkandarasi na Halmashauri kuhakikisha ujenzi wa soko hili unazingatia ubora, kasi na viwango vilivyokubaliwa ili mradi huu wa kimkakati ukamilike kwa wakati na kuwaletea wananchi manufaa yaliyokusudiwa.”Amesema.

Mradi wa ujenzi wa Soko la Kimataifa la Vitunguu unaogharimu zaidi ya Shilingi bilioni 3.9, hadi sasa umefikia asilimia 20 ya utekelezaji, na unatarajiwa kuboresha biashara ya zao la vitunguu, kukuza uchumi wa wakulima na wafanyabiashara pamoja na kuongeza fursa za ajira mara baada ya kukamilika.

“Miradi ya aina hii ina mchango mkubwa katika kuimarisha uchumi wa wananchi na kutekeleza kwa vitendo Ilani ya Chama Cha Mapinduzi, hivyo lazima isimamiwe kwa umakini na uwajibikaji mkubwa.”alisisitiza Kihongosi.

Chama Cha Mapinduzi kitaendelea kusimamia kwa karibu utekelezaji wa miradi ya maendeleo nchini ili kuhakikisha wananchi wananufaika na rasilimali za taifa kwa haki na ufanisi.












Top News