Na Janeth Raphael MichuziTv – Dodoma

Mashirika yasiyo ya kiserikali (AZAKI) yameiomba Serikali kupitia Bunge kuhakikisha asilimia tatu ya mapato ya halmashauri nchini zinatengwa mahsusi kwa ajili ya huduma za ulinzi na usalama wa mtoto, hatua inayolenga kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia na malezi yasiyo salama kwa watoto.

Wito huo umetolewa katika warsha ya wabunge kuhusu masuala ya ulinzi wa mtoto iliyoandaliwa na Shirika la World Vision Tanzania, ambapo Kamati za Kudumu za Bunge za PAC, LAAC pamoja na Kamati ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii zilishiriki kupokea mapendekezo kutoka kwa asasi za kiraia ili kuyafikisha bungeni.

Akizungumza katika warsha hiyo, mwakilishi wa asasi za kiraia, Ombeni Kimaro, alisema bado kuna ongezeko la vitendo vya ukatili dhidi ya watoto katika maeneo mbalimbali nchini, hali inayohitaji hatua za haraka za kisera na kifedha ili kukabiliana nayo.

Amesema ipo haja ya Serikali kuhakikisha fedha hizo zinaingizwa katika bajeti za taifa pamoja na halmashauri ili kuwezesha utekelezaji wa mipango ya ulinzi wa mtoto na huduma za kijamii zinazohusiana na ustawi wa watoto.

“Tunataka kuona suala la ulinzi wa mtoto linapewa uzito wa kitaifa. Halmashauri zitenge fedha maalum kusaidia mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia na kuhakikisha watoto wanakuwa katika mazingira salama,” alisema Kimaro.

Aidha, alisema kupungua kwa misaada kutoka kwa wafadhili wa kimataifa kwa mashirika yanayojihusisha na ulinzi wa mtoto kunapaswa kuwa chachu kwa Serikali kuongeza uwekezaji wa ndani katika sekta hiyo muhimu kwa maendeleo ya taifa.

Kwa mujibu wa Kimaro, kutotengwa kwa fedha hizo kunaweza kuchangia kuongezeka kwa changamoto za malezi, maadili na usalama wa watoto pamoja na vijana nchini.

“Bila kufanya hivyo tunaweza kujikuta tunazalisha kizazi kisicho salama na kisicho na maadili. Ulinzi wa mtoto ni uwekezaji wa moja kwa moja kwa taifa la baadaye,” alisisitiza.

Akizungumza kwa niaba ya wabunge, Mwenyekiti wa Kamati ya PAC, Devotha Minja, alisema kamati hiyo ipo tayari kulisemea suala hilo bungeni ili kuhakikisha mapendekezo hayo yanafanyiwa kazi na fedha zinatengwa katika halmashauri zote nchini.

Kwa upande wake, mwakilishi wa Kamati ya LAAC, Josephine Kapone, alisema kamati hiyo itashirikiana na kamati nyingine kuhakikisha suala la ulinzi wa mtoto linapata usimamizi na utekelezaji unaostahili.

Naye mwakilishi wa Kamati ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii, Kafti Kafti, alisema kamati yao itaendelea kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa mapendekezo hayo kwa kuwa ndiyo yenye dhamana ya moja kwa moja katika masuala ya ustawi wa mtoto.

Mtafiti na mchambuzi kutoka HakiElimu, Joshua Mwakalikamo, alisema tafiti mbalimbali zimekuwa zikionesha umuhimu wa kuwekeza katika ulinzi wa mtoto ili kujenga jamii salama na yenye maadili bora.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Mipango na Udhibiti Ubora wa World Vision Tanzania, AZAKI ZAITAKA SERIKALI KUTENGA 3% KWA ULINZI WA MTOTO.




Na Mwandishi Wetu, Zimbabwe

Tanzania imeendelea kung’ara katika ukanda wa Kusini mwa Afrika baada ya kutajwa kuwa miongoni mwa nchi zinazoongoza kwa mifumo madhubuti ya usimamizi wa maafa, hatua inayozifanya nchi nyingine wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kujifunza kupitia uzoefu wake.

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Kaspar Mmuya wakati akimwakilisha Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Mhe. Balamagamba Kabudi wakati wa Mkutano wa Sita wa Kawaida wa Kamati ya Mawaziri Wanaohusika na Usimamizi wa Maafa kwa nchi wanachama wa SADC unaofanyika mjini Masvingo, Zimbabwe.

Amesema Tanzania imefanikiwa kuimarisha mifumo ya kuzuia, kupunguza madhara, kujiandaa na kurejesha hali baada ya maafa kutokana na uwekezaji mkubwa uliofanywa katika sekta ya uratibu wa maafa nchini.

Kwa mujibu wa Mhe. Mmuya amesema moja ya mafanikio makubwa ni kuanzishwa kwa Kituo cha Ufuatiliaji wa Mwenendo wa Majanga na Tahadhari ya Mapema (National Emergency Operation and Communication Center Situation Room), ambacho kinafanya kazi saa 24 kila siku kufuatilia na kuchambua taarifa za majanga.

“Kwa kupitia kituo hiki, Serikali imeweza kupata taarifa za mapema kuhusu majanga yanayoweza kutokea, kufanya uchambuzi wa madhara na kuweka mikakati ya haraka ya kukabiliana nayo,” alisema Mhe Mmuya

Aliongeza kuwa matumizi ya teknolojia ya kisasa katika ukusanyaji na uchambuzi wa takwimu za wakati halisi yamechangia kuongeza ufanisi wa maamuzi na kurahisisha utoaji wa taarifa rasmi kwa wananchi kuhusu namna ya kujiandaa dhidi ya maafa.

“Tunatumia takwimu za sasa na za zamani kutabiri hatari zinazoweza kujitokeza, jambo ambalo linaisaidia Serikali kupanga kwa usahihi hatua za kurejesha hali na kuendelea kulinda maisha ya wananchi,” alisisitiza.

Aidha, aliwaalika wajumbe kutoka nchi wanachama wa SADC kutembelea Tanzania ili kujionea namna mifumo hiyo inavyofanya kazi pamoja na ubunifu unaotumika katika usimamizi wa maafa.

Mkutano huo wa siku nne umezikutanisha nchi 16 wanachama wa SADC pamoja na wataalamu wa kitaifa na mashirika ya kimataifa kujadili utekelezaji wa programu za kikanda za usimamizi wa maafa na namna ya kuimarisha ushirikiano wa kikanda.

Pamoja na mambo mengine, mkutano huo unatarajiwa kuwa jukwaa muhimu kwa mawaziri na washirika wa maendeleo kujadili uwekezaji katika sekta ya usimamizi wa maafa kwa lengo la kujenga ustahimilivu wa kikanda dhidi ya majanga mbalimbali yanayoendelea kujitokeza duniani.






▪️︎ Dkt. Mwigulu asema Serikali imejipanga kujenga jengo lenye hadhi ya kimataifa

▪️︎ Asema Mwanza itaendelea kuwa kitovu muhimu cha shughuli za kiuchumi Kanda ya Ziwa


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali inaendelea kuchukua hatua kuhakikisha Uwanja wa Ndege wa Mwanza unaboreshwa na kujengwa katika hadhi ya kimataifa ili kuendana na hadhi ya jiji la Mwanza kama kitovu muhimu cha shughuli za kiuchumi Kanda ya Ziwa.

Amesema hayo bungeni jijini Dodoma wakati akitoa kauli ya Serikali kuhusu hoja ya maendeleo ya Uwanja wa Ndege wa Mwanza iliyowasilishwa na Mbunge wa Magu, Mhe. Boniventura Kiswaga, katika mjadala wa bajeti ya Wizara ya Uchukuzi kwenye Kikao cha 28 cha Mkutano wa Tatu wa Bunge la 13, leo Mei 13, 2026.

Waziri Mkuu amesema Serikali inatambua umuhimu wa Uwanja wa Ndege wa Mwanza na imeendelea kufanya jitihada mbalimbali kuhakikisha unakuwa na uwezo wa kuhudumia ndege kubwa pamoja na kukidhi viwango vya kimataifa.

“Zipo jitihada ambazo zimekuwa zikifanyika kuhakikisha kwamba uwanja wa ndege wa Mwanza unaendana na hadhi ya Mwanza kama kitovu cha shughuli za kiuchumi Kanda ya Ziwa,” amesema.

Aidha, Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea na mazungumzo ya kuongeza eneo la uwanja huo ili kuwezesha upanuzi wa njia ya kurukia ndege (runway) pamoja na maboresho mengine muhimu ya miundombinu.

Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu amesema Serikali imekubaliana kujenga jengo jipya la abiria litakalokuwa na hadhi ya kimataifa na kuendana na mahitaji ya muda mrefu ya uwanja huo.

“Imekuja kukubalika kwamba tujenge jengo ambalo halitahitaji kubomolewa tena baada ya muda mfupi, bali jengo lenye hadhi na viwango vya viwanja vya ndege vya kimataifa,” amesema.

Ameongeza kuwa Serikali itaendelea na mpango huo sambamba na utekelezaji wa miradi mingine ya viwanja vya ndege nchini, huku akisisitiza kuwa dhamira ya kuifanya Mwanza kuwa kitovu kikubwa cha uchumi kupitia usafiri wa anga ipo pale pale.

Waziri Mkuu amesema Serikali itafanya kikao maalumu na wabunge wa Mkoa wa Mwanza pamoja na wizara husika ili kuondoa changamoto zilizokuwa zikikwamisha utekelezaji wa mradi huo na kuruhusu hatua zinazofuata kuendelea.


Na Seif Mangwangi, Michuzi TV Arusha

BENKI ya CRDB imetangaza neema kwa wanahisa kwa ongezeko la asilimia 38 kutoka sh.65 ya mwaka jana hadi kufikia sh.90 kwa hisa moja mwaka huu 2026.

Akizungumza na waandishi wa habari kuelekea mkutano mkuu wa 31 wa wanahisa Leo Mei16, 2026 Jijini hapa Mwenyekiti wa bodi ya wakurugenzi wa benki ya CRDB Prof. Neema Mori amesema wanahisa wana mchango mkubwa na ni nguzo ya msingi katika maendeleo endelevu.

Aidha amewakaribisha wanahisa kuhudhuria kwa wingi katika semina na mkutano mkuu wa 31 ili kujifunza, kuweka mikakati ya pamoja, kutambua fursa zilizopo, kukaribisha wanahisa wapya na kufahamishwa fursa mpya.

Profesa Neema amesema katika semina watakayoifanya vijana ndio watapewa kipaumbele huku akisisitiza kuwa vijana ndio nguvu ya uwekezaji katika taifa lolote duniani.

"Kupitia semina hiyo vijana wameandaliwa fursa mpya ya uwezeshwaji katika uwekezaji kuhakikisha wanamiliki uchumi mzuri, Mkutano huu ni muhimu sana kwetu, wadau, wanachama na wanahisa kwa ujumla, " amesema.

Amesema kutakuwa na mada 12 za msingi ambazo zitawafanya kufikia mafanikio ya pamoja na kuwataka wanahisa kuendelea kuiamini benki ya CRDB kwa sababu inazingatia misingi na kanuni.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa benki ya CRDB Dkt. Abdulmajid Nsekela amesema benki hiyo imeendelea kuwa imara na kufanikiwa kuvuna faida ya shilingi bilioni 206 kwa kipindi cha mwaka mmoja.

Hata hivyo ameongeza kuwa, ubunifu umeongezeka, na huduma nyingi kwa sasa zinapatikana nje ya benki.

"Mafanikio ya miaka 30 ijayo yanategemea uwekezaji wa kina kwa vijana wa sasa, tutahakikisha tunakuwa nao karibu ili kuandaa wawekezaji wazuri wa kesho. 

Benki yetu imevuka mipaka na imeendelea kufanya vizuri kimataifa, nawashukiru sana wateja wetu kutuamini na kuwekeza kwetu, Kama kampuni inayomilikiwa kwa mfumo wa hisa, wanahisa wana nafasi ya kupata taarifa, kutoa maoni na kufahamu mustakabali wa benki yao, Wito wangu kwenu vijana changamkieni fulsa ambazo benki yenu imewaletea ili kesho muwe wawekezaji wakuu wa CRDB" amesema Dkt. Nsekela.





 

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amemtembelea na kumjulia hali, Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. John Samwel Malecela katika makazi yake Kilimani Jijini Dodoma leo tarehe 13 Mei 2026.




Na Pamela Mollel,Arusha.

CRDB Bank Plc imezindua rasmi Ripoti ya Mwaka 2025 katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika jijini Arusha, ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea Mkutano Mkuu wa 31 wa Wanahisa wa benki hiyo unaotarajiwa kufanyika Mei 16, 2026 katika Ukumbi wa Simba ndani ya Arusha International Conference Centre (AICC)

Ripoti hiyo imeeleza kwa kina utendaji wa benki, mafanikio yaliyopatikana pamoja na hatua mbalimbali za ukuaji wa biashara na uendelevu zilizotekelezwa katika mwaka uliopita

Akizindua ripoti hiyo, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa CRDB Bank Plc, Profesa Neema Mori, amewataka wanahisa kuisoma kwa makini ili waweze kushiriki kikamilifu katika maamuzi yatakayofanyika kwenye mkutano mkuu ujao.

Prof. Mori amesema Mkutano Mkuu wa 31 wa Wanahisa utafanyika katika ukumbi wa Simba wa AICC pamoja na kupitia njia ya kidijitali, hatua inayolenga kuongeza ushiriki wa wanahisa wengi zaidi waliopo ndani na nje ya nchi

Aidha, amewakaribisha wanahisa wote kushiriki mkutano huo, akisema ni jukwaa muhimu la kujadili maendeleo ya benki pamoja na maamuzi yatakayosaidia kukuza taasisi hiyo kwa miaka ijayo

Akizungumzia Siku ya Uwekezaji kwa Wanahisa itakayofanyika Mei 15, 2026, Prof. Mori amesema mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar

Amesema katika mkutano huo wanahisa watajadili na kuidhinisha agenda mbalimbali zikiwemo Ripoti ya Wakurugenzi, taarifa za hesabu zilizokaguliwa za mwaka 2025, pendekezo la gawio, uteuzi wa wakaguzi wa hesabu pamoja na uteuzi wa mjumbe mmoja huru wa bodi

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Bank Plc, Abdulmajid Nsekela, amesema benki hiyo inaingia kwenye mkutano huo ikiwa na matokeo mazuri ya kifedha na kuendelea kuimarisha nafasi yake katika sekta ya fedha

Dkt. Nsekela amesema katika robo ya kwanza ya mwaka 2026, benki hiyo imefanikiwa kurekodi faida baada ya kodi ya Shilingi bilioni 206, matokeo ambayo yametokana na maamuzi sahihi ya kimkakati, uongozi imara na kuendelea kuimarika kwa imani ya wanahisa na wawekezaji

Akizungumzia kaulimbiu ya mwaka huu ya “Vijana na Uwekezaji katika Hisa,” amesema CRDB Bank Plc inalenga kuhamasisha vijana kuona uwekezaji kama sehemu muhimu ya maisha yao ya baadaye

Amesema benki hiyo imeendelea kuweka mazingira rafiki yatakayowawezesha vijana kujifunza kuhusu uwekezaji katika hisa na masoko ya mitaji ili wawe sehemu ya safari ya ukuaji wa benki hiyo na maendeleo ya kiuchumi kwa ujumla.








Na Janeth Raphael MichuziTv – Dodoma

Serikali kupitia Shirika la Reli Tanzania (TRC) imeendelea kuimarisha huduma za usafiri wa abiria na mizigo kupitia reli ya kisasa ya SGR, huku idadi ya watumiaji wa huduma hiyo ikiendelea kuongezeka kwa kasi.

Akizungumza leo Bungeni jijini Dodoma wakati akiwasilisha hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Ujenzi kwa mwaka wa fedha 2026/27, Waziri wa Ujenzi, Profesa Makame Mbarawa amesema huduma za usafiri kati ya Dar es Salaam na Dodoma zimeendelea kuimarika na kuvutia wananchi wengi zaidi kutumia reli hiyo.

Profesa Mbarawa amesema katika kipindi cha Julai 2025 hadi Machi 2026, jumla ya abiria milioni 2.51 walisafirishwa kupitia reli ya SGR kati ya Dar es Salaam na Dodoma, ikilinganishwa na abiria milioni 2.05 waliosafirishwa katika kipindi kama hicho cha mwaka wa fedha 2024/25.

Amesema ongezeko hilo ni sawa na asilimia 22.40, jambo linaloonesha kuongezeka kwa imani ya wananchi katika huduma za usafiri wa reli ya kisasa nchini.

Aidha, Waziri huyo amesema Serikali imeendelea kutekeleza ahadi yake ya kuanza usafirishaji wa mizigo kupitia reli ya SGR, ambapo katika kipindi cha Julai 2025 hadi Machi 2026, TRC ilisafirisha jumla ya tani 102,452 za mizigo.

Ameeleza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuboresha sekta ya uchukuzi nchini kwa kuongeza ufanisi wa usafirishaji wa abiria na mizigo, pamoja na kuchochea ukuaji wa uchumi kupitia miundombinu ya kisasa ya reli.


Na Mwandishi Wetu, Michuzi TV 

SERIKALI kupitia Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), imeendelea kuimarisha utoaji na udhibiti wa huduma za hali ya hewa nchini kwa lengo la kuongeza usalama, ufanisi na maendeleo katika sekta mbalimbali, ikiwemo usafiri wa anga.

Hayo yameelezwa leo Mei 13, 2026 Bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa, wakati akiwasilisha makadilio ya mapato na matumizi ya Wizara hiyo.

Profesa Mbarawa amesema TMA imekamilisha ufungaji wa mitambo miwili ya uangazi wa hali ya hewa katika Uwanja wa Ndege wa Mpanda na Pemba kwa lengo la kuboresha huduma za hali ya hewa kwa sekta ndogo ya usafiri wa anga.

Amesema mitambo hiyo itasaidia kuongeza usahihi wa taarifa za hali ya hewa zinazotolewa kwa marubani pamoja na wadau wengine wa usafiri wa anga, hatua itakayochangia kuimarisha usalama wa safari za ndege na kupunguza changamoto zinazoweza kusababishwa na mabadiliko ya hali ya hewa.

Aidha, amesema TMA inaendelea na ujenzi wa miundombinu muhimu ya hali ya hewa ikiwemo maabara ya uhakiki wa vifaa vya hali ya hewa (Calibration Center) jijini Dar es Salaam, ambapo ujenzi wake umefikia asilimia 46.

“Ujenzi wa maabara hiyo ni hatua muhimu katika kuhakikisha vifaa vya hali ya hewa vinakuwa na ubora na usahihi unaohitajika katika utoaji wa taarifa za hali ya hewa nchini,” amesema Profesa Mbarawa.

Ameongeza kuwa uwekezaji huo unaonesha dhamira ya Serikali ya kuendelea kuimarisha sekta ya hali ya hewa ili kuendana na maendeleo ya teknolojia pamoja na mahitaji ya sekta mbalimbali zinazotegemea taarifa sahihi za hali ya hewa nchini.




Ujumbe wa Tanzania
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassanakiwa kwenye mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa Kituo cha Afrika cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa (Africa CDC), Dkt. Jean Kaseya pamoja na Ujumbe wake, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 13 Mei, 2026. 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Mkurugenzi Mkuu wa Kituo cha Afrika cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa (Africa CDC), Dkt. Jean Kaseya pamoja na Ujumbe wake Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 13 Mei, 2026.
 



Mke wa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Bi. Neema Mwigulu Nchemba, ametoa wito kwa viongozi na wadau wa Afrika kuweka kipaumbele katika ulinzi wa watoto dhidi ya ukatili wa kidijitali.

Akizungumza jijini Nairobi, Kenya Mei 12, 2026, katika Mkutano wa Wenza wa Mawaziri wakuu wa nchi za Afrika, uliofanyika Pembezoni mwa Mkutano wa “Africa-Forward Summit” ukilenga kujenga mazingira salama ya kidijitali kwa watoto wa Afrika katika ulimwengu unaoendeshwa na Akili Unde (AI). Bi.Nchemba alisisitiza kuwa mustakabali wa bara la Afrika hautategemea tu vigezo vya kiuchumi, bali uwezo wa watoto kujifunza na kuvumbua katika nafasi ya kidijitali bila hofu ya unyanyasaji.

Katika hotuba yake, alibainisha kuwa ingawa teknolojia ya Akili Bandia (AI) inatoa fursa kubwa katika sekta za elimu, afya, na ujasiriamali, imeleta pia hatari mpya na halisi. Alitaja changamoto kama vile uonevu mtandaoni, unyanyasaji wa kijinsia unaochochewa na AI, na ulaghai kama vitisho vinavyovuruga utu na maendeleo ya watoto barani Afrika.

Ameeleza hatua zilizopigwa na Tanzania, ikiwemo kufanya marekebisho ya Sheria ya Mtoto (Sura ya 13) na kuimarisha utekelezaji wa Sheria ya Makosa ya Mtandao ya mwaka 2015. Aidha, alikumbusha Kampeni ya Kitaifa ya Ulinzi wa Watoto Mtandaoni iliyoanzishwa Februari 2024 na kuundwa kamati maalum ya wadau mbalimbali ili kuhakikisha mazingira salama kwa watoto.

Mkutano huo, uliandaliwa na Kuongozwa na Mke wa Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mama Rachel Ruto ambapo ulihitimishwa kwa wito wa dharura wa kuimarisha ushirikiano wa kikanda na sheria madhubuti.















KAMPUNI ya utoaji wa huduma za bima ya afya kwa waajiri, Vitality Health International (Africa), imebadilisha rasmi jina na sasa itafahamika kama Discovery Health – Global Health Solutions, hatua inayolenga kuimarisha utoaji wa huduma za afya kwa waajiri na wafanyakazi wao nchini Tanzania na katika bara la Afrika kwa ujumla.

Mabadiliko hayo yameanza rasmi Januari 1, 2026, huku kampuni hiyo ikieleza kuwa hatua hiyo inalenga kuendeleza huduma zake za afya kwa kuunganisha uzoefu wake wa muda mrefu na programu ya ustawi ya Vitality pamoja na teknolojia za kisasa za huduma za afya.

Akizungumza Johannesburg, Afrika Kusini, Mkurugenzi Mkuu wa Discovery Health – Global Health Solutions, Emma Knox, alisema licha ya kubadilika kwa jina la kampuni, dhamira yao ya kuhakikisha watu wanakuwa na afya bora na maisha yenye ustawi itaendelea kuwa ile ile.

“Ingawa jina letu linabadilika, ahadi yetu kwa wateja wetu na kusudi letu la msingi la kuwafanya watu wawe na afya njema na kulinda maisha yao vinaendelea kubaki vilevile,” alisema Knox.

Alieleza kuwa mabadiliko hayo yatawezesha kampuni hiyo kuimarisha ushirikiano wake na kampuni za bima za ndani barani Afrika pamoja na kuleta suluhisho mpya za afya zinazolenga mahitaji halisi ya waajiri na wafanyakazi wao.

Nchini Tanzania, kampuni hiyo itaendelea kushirikiana na Strategis Insurance, ushirikiano ulioanza mwaka 2024, kwa lengo la kutoa huduma bora za afya zinazokidhi mazingira ya ndani ya huduma za afya na mahitaji ya waajiri wa Kitanzania.

Kwa mujibu wa Knox, ushirikiano huo umeiwezesha kampuni kupanua huduma zake nchini huku ikiendelea kutoa suluhisho za afya zenye kuzingatia mahitaji ya soko la ndani.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Strategis Insurance, Dk. Malav Manek, alisema wana matumaini makubwa ya kuendelea kuimarisha ushirikiano huo kupitia Discovery Health – Global Health Solutions.

“Tunaendelea kujizatiti kutoa bidhaa za kibunifu zinazolenga kukidhi mahitaji ya wateja huku tukihakikisha kiwango cha juu cha huduma kwa wateja wetu,” alisema Dk. Manek.

Kupitia mfumo wake mpya wa Global Health Solutions, kampuni hiyo itaendelea kutoa huduma za usimamizi wa afya na “managed care” kwa kutumia uzoefu wa zaidi ya miaka 34 wa Discovery Health katika sekta ya afya nchini Afrika Kusini.

Discovery Health pia imeeleza kuwa itaendelea kuweka mkazo katika usimamizi bora wa huduma za matibabu, udhibiti wa hatari pamoja na matumizi ya mifumo ya kisasa ya taarifa za afya ili kuhakikisha wateja wanapata huduma bora kwa gharama endelevu.


▪️︎ Asema Serikali inalenga kupunguza utegemezi wa kuagiza dawa kutoka nje

▪️︎ Aisisitiza Afrika kuongeza thamani ya malighafi na kuimarisha uhamishaji wa teknolojia


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Tanzania imeweka kipaumbele katika uwekezaji wa viwanda vya dawa nchini ili kupunguza utegemezi wa kuagiza dawa kutoka nje ya nchi.

Dkt. Mwigulu amesema hayo jijini Nairobi, Kenya alipokutana na Afisa Mtendaji Mkuu wa Shirika la Maendeleo la Ufaransa (AFD), Christophe Lecourtier, kando ya Mkutano wa Ushirikiano kati ya Afrika na Ufaransa (Africa Forward Summit).

“Tunaagiza kiasi kikubwa cha dawa kutoka nje ya nchi, lakini sasa tumeweka kipaumbele kuona jinsi tunavyoweza kuwekeza kwenye viwanda vya dawa ili tuzalishe hapa nchini,” amesema Dkt. Nchemba.

“Kupitia ofisi yako pamoja na wadau wengine, wanaweza kutumia fursa hii kubwa iliyopo kuja kuwekeza kwenye eneo hilo. Na kama unavyofahamu, kuwekeza Tanzania ni kuingia katika lango la ukanda wa Afrika Mashariki (EAC) pamoja na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC).”

Aidha, Dkt. Mwigulu amepongeza dhamira ya AFD ya kuusaidia Mradi wa Maji wa Ziwa Victoria Awamu ya Pili, akieleza kuwa mradi huo ni wa kimkakati katika kuboresha upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea kutoa kipaumbele katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo ikiwemo reli ya kisasa ya SGR, nishati, kilimo hususan umwagiliaji pamoja na sekta ya afya kupitia uwekezaji katika uzalishaji wa dawa nchini.

Kadhalika, Waziri Mkuu ameishukuru AFD kwa kuendelea kushirikiana na Tanzania katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo nchini.

“Tunathibitisha tena dhamira ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuendelea kufanya kazi kwa karibu na AFD kwa manufaa ya maendeleo ya wananchi wetu,” amesema.

Akizungumza katika mjadala kuhusu maendeleo ya sekta ya kilimo, Dkt. Mwigulu ametoa wito kwa wadau wa maendeleo kuoanisha malengo ya Bara la Afrika ili kuchochea maendeleo endelevu.

“Tumekaa muda mrefu tukizungumzia kujenga uwezo badala ya kujenga miundombinu itakayowezesha bara letu na nchi zetu kuendesha ajenda zao ipasavyo,” amesema.

Aidha, Waziri Mkuu alisisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano katika uhamishaji wa teknolojia na matumizi ya mifumo ya kisasa ya kilimo.

“Tunatarajia ushirikiano katika uhamishaji wa teknolojia ikiwa ni pamoja na uendelezaji wa matumizi ya zana za kisasa za kilimo, utekelezaji wa huduma za ugani na mifumo ya kidijitali. Si muda sasa wa kusafirisha malighafi nje ya nchi, tunataka mwelekeo wetu uwe kwenye kuongeza thamani,” amesema.

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba alimuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Mkutano wa Ushirikiano kati ya Afrika na Ufaransa uliofanyika Mei 11 hadi 12, 2026 jijini Nairobi, Kenya. 








Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Wizara ya Uchukuzi imewasilisha ombi la kuidhinishiwa bajeti ya jumla ya Shilingi 2,872,738,082,000 kwa mwaka wa fedha 2026/27, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa mipango ya kuimarisha na kuendeleza sekta ya uchukuzi nchini.

Kwa mujibu wa makadirio hayo, kati ya fedha hizo, Shilingi 126,041,236,000 zimetengwa kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida, huku Shilingi 2,746,696,846,000 zikielekezwa katika Miradi ya Maendeleo, ikilenga kuboresha miundombinu ya usafiri wa anga, reli, barabara na huduma nyingine za uchukuzi.

Akizungumza bungeni jijini Dodoma wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya wizara hiyo, Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa, amesema kuwa bajeti hiyo imelenga kuharakisha utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya sekta ya uchukuzi nchini, sambamba na kuongeza ufanisi wa huduma za usafiri.

Ameeleza kuwa pamoja na hotuba hiyo, wizara imeambatisha majedwali mbalimbali yenye takwimu na taarifa za kina ili kutoa uelewa mpana zaidi kwa Waheshimiwa Wabunge na wananchi kuhusu hali ya utekelezaji wa sekta hiyo.

Aidha, amesema majedwali hayo ni sehemu ya hotuba rasmi ya bajeti na yanapatikana pia kupitia tovuti ya Wizara ya Uchukuzi kwa ajili ya rejea ya umma kupitia www.uchukuzi.go.tz.

Wizara hiyo inaendelea kuweka mkazo katika kuboresha miundombinu ya uchukuzi ili kuchochea ukuaji wa uchumi na kurahisisha usafirishaji wa watu na bidhaa nchini.



Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Serikali imewataka vijana wa Kitanzania kujiepusha na ushawishi wa kujiingiza katika migogoro ya kivita ya kimataifa kwa lengo la kutafuta kipato, ikionya kuwa hatua hiyo ni kinyume cha sheria na inaweza kuhatarisha maisha yao.

Onyo hilo limetolewa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Ngwaru Maghembe wakati akijibu swali la Mbunge Jesca John Magufuli aliyehoji Serikali ina mkakati gani wa kujenga uelewa kwa vijana kuhusu athari za kushiriki katika migogoro ya kimataifa, ikiwemo vita kati ya Ukraine na Urusi.

Dkt. Maghembe amesema katika kipindi cha hivi karibuni kumekuwepo na mwenendo wa baadhi ya vijana, hususan kutoka Bara la Afrika, kuhamasishwa kujiunga na majeshi ya nchi zinazokabiliwa na migogoro ya kivita kwa ahadi ya ajira na kipato bora kutokana na changamoto za ukosefu wa ajira katika nchi zao.

Amesema Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kutoa elimu ya uraia na kuongeza uelewa kwa vijana kuhusu madhara ya kujiingiza katika vita vya nje, ikisisitiza kuwa kushiriki katika migogoro hiyo bila utaratibu rasmi ni kinyume cha sheria za Tanzania pamoja na sheria za kimataifa.

“Vijana wanapaswa kuelewa kuwa migogoro ya kimataifa ina athari kubwa kiusalama, kijamii na kiuchumi, na kwa baadhi inaweza kusababisha vifo, majeraha makubwa au ulemavu wa kudumu,” amesema Dkt. Maghembe.

Ameeleza kuwa juhudi hizo zinaongozwa na miongozo mbalimbali ya kitaifa ikiwemo Sera ya Mambo ya Nje ya mwaka 2001 Toleo la 2024 pamoja na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambazo zinahimiza usalama, ustawi wa vijana na ushiriki wao katika shughuli halali za maendeleo.

Wakati huo huo, Serikali imeendelea kuratibu upatikanaji wa ajira salama kwa vijana nje ya nchi kupitia mikataba ya ushirikiano wa kikanda na kimataifa inayolenga kuhakikisha Watanzania wanapata fursa za kazi katika mazingira yanayolindwa kisheria.

Dkt. Maghembe amesema katika mwaka huu wa fedha, Serikali imefanikisha upatikanaji wa nafasi 1,500 za ajira kwa madereva nchini Qatar pamoja na nafasi nyingine 300 za wauguzi nchini Saudi Arabia.

Aidha, amesema Serikali inaendelea kutekeleza programu mbalimbali za kuwawezesha vijana kiuchumi, ikiwemo kutenga shilingi bilioni 200 kwa ajili ya mikopo ya vijana sambamba na programu maalum za kisekta zinazolenga kuongeza ushiriki wao katika shughuli za uzalishaji na ajira rasmi.

Amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kuhamasisha vijana kutumia fursa halali za kiuchumi zilizopo ndani na nje ya nchi badala ya kujiingiza katika shughuli zinazoweza kuhatarisha usalama na mustakabali wao.




Top News