Na Mwandishi Wetu, Pwani

MPANGO wa Rafiki wa Binti umezindua wimbo maalumu wa  kielimu wa Afya ya Hedhi ikiwa ni kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Afya ya Hedhi Mei 28, 2026.

Taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na Saumu Zidadu, ambaye ni Mratibu wa Mpango wa Rafiki wa Binti, amesema pia wamepanua kuongeza usambazaji wa chupi maalumu za hedhi zinazoweza kutumika tena Tanzania.

“Katika kuadhimisha Siku ya Afya ya Hedhi tarehe 28 Mei, Rafiki wa Binti imetoa wimbo mpya wa kielimu wa uhuishaji unaolenga kuwapa wanafunzi wa kike elimu kuhusu afya ya hedhi pamoja na kuhamasisha kujiamini, heshima na mahudhurio shuleni.

“Wimbo huo umeimbwa na kuandikwa na mwimbaji maarufu wa Tanzania Ashura Kitenge, na ni sehemu ya mpango mpana wa elimu ya afya ya hedhi wa Rafiki wa Binti, ambao huwafundisha wasichana namna sahihi ya kutumia, kufua na kutunza chupi maalumu za hedhi zinazoweza kutumika tena suluhisho bunifu na endelevu linalowasaidia wasichana kujisimamia hedhi zao kwa usalama na kujiamini,”imesema taarifa hiyo ya Zidadu.

Kwa upande wake Nancy Bondo, ambaye ni Mkurugenzi wa Rafiki wa Binti, amesema chupi maalumu za hedhi zinazoweza kutumika tena, ni suluhisho jipya na la kipekee katika jamii nyingi za Tanzania na zimekuwa sehemu muhimu ya kazi ya Rafiki wa Binti katika kusaidia wasichana kuendelea na masomo yao na kupunguza unyanyapaa unaohusiana na hedhi.

“Kupitia mpango wake wa Pakiti za Binti, Rafiki wa Binti tayari imetoa zaidi ya jozi 24,000 za chupi maalumu za hedhi zinazoweza kutumika tena kwa wanafunzi wa kike katika maeneo ya Mafinga, Kilwa Masoko, Mkoa wa Kagera na Zanzibar. Chupi hizo zinaweza kutumika tena kwa miaka miwili au zaidi,” amesema na kuongeza:

Kila Pakiti ya Binti ina jozi sita za chupi maalum za hedhi zinazoweza kutumika tena, elimu ya afya ya hedhi, mifuko ya kuhifadhia vifaa vilivyo vikavu na vyenye unyevunyevu

“Jozi nyingine 24,000 za chupi zinatarajiwa kusambazwa katika utekelezaji wa programu zijazo ndani ya miezi michache ijayo wakati taasisi hiyo ikiendelea kupanua huduma zake kote nchini Tanzania. Afya ya hedhi inahusu elimu na fursa,” amesema Nancy Bondo. 

Amesema mrejesho kutoka serikalini, kwa walimu na wanafunzi kuhusu Mradi wa Binti umekuwa mazuri sana na unawasaidia wasichana kuendelea kuhudhuria shule wakati wa hedhi zao kwa heshima na kujiamini.

"Rafiki wa Binti inajivunia kuwa mshirika rasmi wa Siku ya Afya ya Hedhi na mwanachama wa Muungano wa Afya ya Hedhi Tanzania, ikifanya kazi pamoja na Serikali na wadau mbalimbali nchini kuboresha uelewa na upatikanaji wa huduma za afya ya hedhi,” amesema.

Amesema Rafiki wa Binti ni mpango unaolenga Tanzania, unaosaidia wasichana kupitia elimu ya afya ya hedhi na utoaji wa chupi maalum za hedhi zinazoweza kutumika tena ili kuwasaidia wasichana kubaki shuleni, kuwa na nguvu na kujiamini.

Amesema Rafiki wa Binti ni programu ya Rafiki Australia Tanzania, taasisi inayoendeshwa kwa kujitolea kwa asilimia 100 na iliyosajiliwa Australia na Tanzania.





Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Serikali kupitia Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora imewataka Wakuu wa Idara za Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu katika taasisi za umma kuhakikisha wanashiriki wenyewe katika kikao kazi cha kitaifa kitakachofanyika jijini Dodoma kuanzia Juni 1 hadi 3, 2026, bila kukosekana wala kutuma wawakilishi.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma, Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo, Juma Mkomi amesema kikao hicho ni muhimu katika kuimarisha ufanisi wa utendaji wa rasilimaliwatu serikalini, hivyo kinahitaji ushiriki wa moja kwa moja wa viongozi wote husika.

Amesema kikao hicho kitawakutanisha Wakurugenzi na Wakuu wa Idara za Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu kutoka Wizara mbalimbali, Idara zinazojitegemea, Wakala za Serikali, Mashirika ya Umma, Sekretarieti za Mikoa pamoja na Mamlaka za Serikali za Mitaa, kwa lengo la kujadili mikakati ya kuongeza uwajibikaji, ufanisi na nidhamu ya utendaji katika Utumishi wa Umma.

Mkomi amesema kikao hicho kitafanyika katika Ukumbi wa Mabele Hall jijini Dodoma chini ya kaulimbiu isemayo:

“Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu katika Utumishi wa Umma Ulio Sikivu, Jumuishi, wenye Matokeo na Uwajibikaji Kuelekea Dira 2050.”

Amefafanua kuwa moja ya ajenda kuu zitakazojadiliwa ni matumizi ya mifumo ya kidijiti katika usimamizi wa rasilimaliwatu, ikiwemo mifumo ya e-Uhamisho, e-Watumishi, e-Utendaji, e-Mrejesho pamoja na HR Assessment, ambayo inalenga kuongeza uwazi, ufanisi na uwajibikaji katika taasisi za umma.

Kwa mujibu wa Katibu Mkuu huyo, mifumo hiyo ya kidijiti ni sehemu ya maboresho makubwa yanayoendelea serikalini ili kuendana na mabadiliko ya kiteknolojia pamoja na kutimiza vipaumbele vya Taifa kuelekea Dira ya Maendeleo 2050.

Aidha, amesisitiza kuwa viongozi wote watakaohudhuria watapatiwa maelekezo mahsusi kuhusu usimamizi bora wa rasilimaliwatu serikalini, huku akibainisha kuwa hakutakuwa na nafasi ya uwakilishi, kutokana na umuhimu na uzito wa maudhui yatakayojadiliwa katika kikao hicho.

“Ni muhimu kila kiongozi anayehusika kuhudhuria mwenyewe ili kupata uelewa wa moja kwa moja na maelekezo ya kimkakati kuhusu maboresho ya sekta ya rasilimaliwatu,” ameweka msisitizo Mkomi.

Vilevile, kikao hicho kinatarajiwa kufunguliwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Jakaya Kikwete, ambaye anatarajiwa kutoa mwelekeo wa serikali kuhusu maboresho ya utumishi wa umma na usimamizi wa rasilimaliwatu nchini.

Serikali imesema kikao hicho ni sehemu ya juhudi za kuimarisha utawala bora, kuongeza uwajibikaji wa watumishi wa umma na kuhakikisha taasisi za serikali zinaendeshwa kwa ufanisi unaozingatia matokeo.





Na Mwandishi Wetu

BABATI — Mahakama ya Mwanzo Wilaya ya Babati mkoani Manyara imesitisha kusikiliza kesi ya jinai namba 291 ya mwaka 2026 iliyofunguliwa na aliyekuwa Mbunge wa Babati Mjini, Paulina Gekul, inayomkabili Brayton Lucas (17), baada ya kujiridhisha kuwa mshtakiwa huyo ni mtoto mwenye umri wa chini ya miaka 18 na hivyo shauri hilo linapaswa kusikilizwa katika Mahakama ya Watoto kwa mujibu wa sheria.

Uamuzi huo ulitolewa baada ya Wakili wa upande wa utetezi, Thadei Lister, kuiomba mahakama kujiridhisha kuhusu umri wa mshtakiwa kwa kuwasilisha nyaraka mbalimbali ikiwemo cheti cha kuzaliwa kilichoonesha kuwa Brayton alizaliwa Novemba 12, 2008 na kwa sasa ana umri wa miaka 17 na miezi sita, tofauti na taarifa zilizokuwa katika hati ya mashtaka zilizomtaja kuwa na miaka 19.

Katika shauri hilo, Paulina Gekul alidai kuwa Brayton Lucas, ambaye alikuwa akichunga mifugo yake, alihusika katika wizi wa mbuzi 15 wenye thamani ya shilingi milioni tatu, kosa linalodaiwa kufanyika chini ya kifungu cha 268 cha sheria ya wizi wa mifugo. Kesi hiyo ilikuwa na jumla ya watuhumiwa watatu.

Mahakama pia ilielezwa kuwa mtoto huyo alikuwa amechanganywa katika shauri moja na watuhumiwa watu wazima, jambo ambalo upande wa utetezi ulidai ni kinyume na sheria zinazolinda haki za mtoto.

Baada ya kupitia nyaraka zilizowasilishwa, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Babati, Ahmed Mgodo, alisema mahakama imejiridhisha kuwa Brayton Lucas ni mtoto na hivyo haina mamlaka ya kuendelea kusikiliza kesi hiyo. Kutokana na uamuzi huo, mahakama ilisimamisha shauri hilo dhidi ya mshtakiwa huyo na kuagiza polisi kuandaa hati mpya ya mashtaka kwa mujibu wa sheria zinazohusu watoto.

Brayton Lucas alipatiwa dhamana huku washtakiwa wawili wengine wakiendelea kushikiliwa. Wakili Thadei Lister amesema wako tayari kuendelea kumtetea mtoto huyo iwapo atafikishwa katika Mahakama ya Watoto.

Akizungumza nje ya mahakama, Wakili Thadei alisema Brayton ni mwanafunzi wa kidato cha nne ambaye alitoweka akiwa Wilaya ya Arumeru mkoani Arusha na wazazi wake walikuwa wakimtafuta kwa kipindi cha miezi mitatu kabla ya kupata taarifa kuwa amekamatwa Babati kwa tuhuma za wizi.

Mama mzazi wa Brayton alisema mtoto wake alitakiwa kuwa shuleni baada ya kumaliza kidato cha nne na tayari alikuwa amepangiwa shule, lakini aliondoka nyumbani bila kutoa taarifa na baada ya juhudi za muda mrefu za kumtafuta walipata taarifa kuwa alikuwa Babati akifanya kazi.

Wakati huo huo, Diwani wa Kata ya Maruvango Wilaya ya Arumeru Mashariki, Digna Nassari, amesema taarifa za kupotea kwa mtoto huyo zilikuwa zimetolewa polisi miezi mitatu kabla ya kufunguliwa kesi dhidi yake na Paulina Gekul.

Aidha, Digna amesema Brayton ni miongoni mwa watoto 16 kutoka kata hiyo waliotoroka shule, huku akisisitiza umuhimu wa jamii kushirikiana kuhakikisha watoto wanarudi katika mfumo wa elimu na kupata ulinzi unaostahili.

Na Mwandishi wetu - Msumbiji

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Dkt. Jim Yonazi ameupongeza Ubalozi wa Tanzania nchini Msumbiji kwa namna unavyoendelea kutekeleza majukumu yake na kuimarisha mahusiano baina ya nchi hizo mbili.

Ametoa pongezi hizo alipotembelea ofisi hizo pamoja na ujumbe alioongozana nao kwa lengo la kushiriki katika ziara ya kubadilishana uzoefu kati ya Tanzania na Msumbiji kuhusu hatua za mapema kabla ya majanga unaoendelea kwa siku tano kuanzia tarehe 25 hadi 29 Mei, 2026 Mjini Maputo Msumbiji.

Dkt. Yonazi amezungumza na watumishi wa ubalozi huo na kupokea taarifa fupi ya utekelezaji wa majukumu ya Ubalozi iliyotolewa na Mwambata fedha Bw. Samson Marwa kwa niaba ya Mhe. CP. Hamad Khamis Hamad, Balozi wa Tanzania nchini Msumbiji ambaye alikuwa katika majukumu mengine.

Aidha, amewashukuru watumishi wa ubalozi huo kwa namna wanavyoendelea kutekeleza majukumu ya msingi huku wakiiwakilisha nchi na kutekeleza diplomasia ya uchumi kwa vitendo.

“Ninawapongeza namna mnavyoendelea kuiwakilisha nchi yetu, ni vyema kuendelea kuangalia fursa zilizopo na kuzitangaza hususan za kiuchumi zitakazowavutia kuja kuwekeza Tanzania, niwasihi kuendelea kuwa mabalozi wazuri wa nchi yetu,” alisema Dkt. Yonazi

Kwa upande wake Mwambata fedha wa ubalozi huo Bw.Samson Marwa akizungumza kwa niaba ya Balozi wa Tanzania nchini Msumbiji alimshukuru Katibu Mkuu huyo kwa kutenga muda wake na kuzitembelea ofisi za ubalozi huku akiahidi kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na kuhakikisha jukumu la msingi la kuhakikisha uhusiano kati ya Tanzania na Msumbiji linaendelea kuimarika kwa manufaa ya nchi hizo mbili.

“Tunashukuru kwa ziara hii muhimu kwetu, mnapotembelea ofisi zetu za ubalozi inaonesha kujali na kutambua kazi zinazofanywa, tunaahidi kuendeleza diplomasia na kuitangaza nchi yetu na fursa zilizopo Tanzania,” alisema Marwa

Sambamba na hilo alieleza dhamira ya kuimarisha ushirikiano wa kihistoria na wa kidugu kati ya Tanzania na Msumbiji huku akisisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano kati ya nchi hizo mbili kwa kuzingatia mchango wa Tanzania kwa Taifa hilo.








Na Janeth Raphael -MichuziTv Bungeni,Dodoma

Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imeeleza kuwa vipaumbele vyake kwa mwaka wa fedha 2026/2027 vitaendelea kutekelezwa kwa kuzingatia miongozo ya kitaifa, kikanda na kimataifa inayolenga kuimarisha maendeleo endelevu na ushirikiano wa kimataifa.

Akizungumza Bungeni, leo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Mahmoud Thabit Kombo (Mb.), amesema wizara hiyo itaongozwa na nyaraka mbalimbali za kimkakati zikiwemo Sera ya Mambo ya Nje ya mwaka 2001, toleo la mwaka 2024, pamoja na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Aidha, amesema utekelezaji wa vipaumbele hivyo pia utazingatia Dira ya Maendeleo ya Zanzibar 2050 pamoja na Mpango wa Nne wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2026/2027 – 2030/2031), ambao unalenga kuimarisha uchumi na ustawi wa wananchi kupitia sekta mbalimbali za maendeleo.

Kwa mujibu wa Waziri Kombo, mipango hiyo pia itaendana na Mpango wa Maendeleo wa Zanzibar (2021–2026) pamoja na Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, ambayo imeweka malengo ya kimkakati ya maendeleo ya taifa katika kipindi kijacho.

Katika hatua nyingine, Wizara hiyo itaendelea kuzingatia mikataba ya kikanda na kimataifa ikiwemo Mkataba wa Jumuiya ya Afrika Mashariki wa mwaka 1999, Mkataba wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) wa mwaka 1992, pamoja na Ajenda ya Umoja wa Mataifa ya Maendeleo Endelevu 2030.

Vilevile, utekelezaji wa vipaumbele hivyo utaongozwa na Ajenda ya Umoja wa Afrika 2063, Dira ya SADC ya mwaka 2050 na Dira ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya mwaka 2050, sambamba na mikataba mingine ya kikanda na kimataifa inayolenga kuimarisha ushirikiano wa mataifa.

Waziri Kombo amebainisha kuwa Wizara pia itaendelea kuzingatia maelekezo ya viongozi wakuu wa kitaifa pamoja na ushauri unaotolewa na Bunge katika kuhakikisha sera na mikakati ya diplomasia ya nchi inatekelezwa kwa ufanisi.

Kwa mujibu wake, vipaumbele vya Wizara kwa mwaka wa fedha 2026/2027 vitajikita katika maeneo makuu manne, ambayo ni kuimarisha uratibu na ushirikiano wa nchi mbili, kikanda na kimataifa, pamoja na kusimamia utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje ya mwaka 2001 (toleo la 2024), hususan katika eneo la diplomasia ya uchumi.

Maeneo mengine ni kulinda taswira, heshima na maslahi ya Taifa katika nyanja za kimataifa, pamoja na kuboresha mazingira ya utendaji kazi kwa watumishi wa Wizara, kuimarisha utawala bora, rasilimali watu na utekelezaji wa miradi ya maendeleo ndani ya Wizara na taasisi zake.

Hatua hiyo inalenga kuimarisha nafasi ya Tanzania katika majukwaa ya kimataifa sambamba na kukuza ushirikiano wa kiuchumi, kisiasa na kijamii kwa manufaa ya wananchi.







Bagamoyo, Pwani

HISTORIA ya ustaarabu wa pwani ya Afrika Mashariki imeendelea kuvutia wageni na watalii wa ndani baada ya ujumbe kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi mkoani Mbeya kutembelea Magofu ya Kaole yaliyopo Bagamoyo mkoani Pwani na kueleza kuvutiwa na urithi mkubwa wa kihistoria uliopo eneo hilo.

Ujumbe huo umetembelea eneo hilo ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha utalii wa ndani na kujifunza historia ya taifa, huku viongozi wake wakieleza kuwa Magofu ya Kaole ni miongoni mwa maeneo yanayoonesha mchango mkubwa wa Tanzania katika historia ya biashara, dini na ustaarabu wa Afrika Mashariki tangu karne ya 13.

Katika ziara hiyo, wageni hao walipata fursa ya kutembelea misikiti ya kale inayosadikiwa kuwa miongoni mwa misikiti ya mwanzo kabisa Afrika Mashariki, makaburi ya kihistoria ya Shirazi yaliyojengwa kwa mawe ya matumbawe, kisima cha kale pamoja na mabaki ya mji wa zamani wa biashara uliokuwa ukiunganisha Afrika, Uarabuni na Asia kupitia Bahari ya Hindi.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, Dk. Libamba Shobo alisema Kaole ni eneo lenye thamani kubwa ya kihistoria na kitamaduni ambalo linaweza kuwa chachu ya kukuza utalii wa ndani na kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu historia ya taifa.

Alisema vivutio vilivyopo katika eneo hilo vinaakisi namna Tanzania ilivyokuwa kitovu muhimu cha biashara na mwingiliano wa tamaduni mbalimbali kwa karne nyingi, hali inayopaswa kutumiwa kuhamasisha kizazi cha sasa kuthamini urithi wa nchi.

“Kaole si eneo la kawaida; ni sehemu inayobeba historia ya taifa letu na ustaarabu wa mwambao wa Afrika Mashariki. Watanzania wengi wanapaswa kufika hapa kujifunza na kutambua mchango wa maeneo haya katika historia yetu,” alisema.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa kuendelea kuhifadhi maeneo ya kihistoria na kuyaendeleza ili yaweze kuchangia zaidi katika uchumi kupitia sekta ya utalii, sambamba na kutoa elimu kwa jamii kuhusu urithi wa Tanzania.

Kwa miaka ya karibuni, Magofu ya Kaole yameendelea kuvutia wageni kutoka ndani na nje ya nchi kutokana na historia yake ya kipekee inayohusisha ustaarabu wa Waswahili, biashara za kale za Bahari ya Hindi pamoja na kuenea kwa dini ya Kiislamu katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Bagamoyo, ambayo kihistoria ilitumika kama lango muhimu la biashara na utamaduni wa pwani, inaendelea kujijengea sifa kama moja ya maeneo muhimu ya utalii wa kihistoria nchini.



Timu ya wataalamu kutoka Makao Makuu ya Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO) kutoka Roma, Italia pamoja na Harare, Zimbabwe, imevutiwa na vivutio vya utalii vilivyopo mkoani Tabora baada ya kutembelea maeneo mbalimbali ya kihistoria na hifadhi za asili zilizopo chini ya usimamizi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS).

Wataalamu hao wanne waliwasili mkoani Tabora Mei 24, 2026 kwa ajili ya kukagua utekelezaji wa Mradi wa Usimamizi Shirikishi wa Misitu ya Miombo katika Nyanda Kame za Magharibi mwa Tanzania (Integrated Landscape Management of Dry Miombo Woodland in the Western Parts of Tanzania), unaotekelezwa kwa ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania na FAO.

Baada ya shughuli za kikazi, ujumbe huo ulipata fursa ya kutembelea vivutio vya utalii vilivyopo katika Ofisi ya Uhifadhi wa Misitu ya Asili Kanda ya Magharibi (DFC Tabora), ikiwemo Hifadhi ya Msitu wa Bwawa la Igombe pamoja na eneo la kihistoria la Tembe la Kwihara.

Wageni hao walieleza kufurahishwa kwao na namna safari hiyo ilivyoandaliwa kwa ustadi mkubwa, wakisifia mchanganyiko wa burudani, elimu na utalii wa asili uliowawezesha kujifunza zaidi kuhusu utajiri wa mazingira na historia ya Tanzania wakati wa utekelezaji wa majukumu yao ya kikazi.

Aidha, walieleza kuwa uzoefu walioupata katika kanda ya Magharibi umeonesha namna miradi ya uhifadhi wa mazingira inavyoweza kwenda sambamba na kukuza utalii endelevu na kuongeza thamani ya rasilimali za misitu nchini.





Na Janeth Raphael MichuziTv Bungeni - Dodoma

WIZARA ya Mifugo na Uvuvi imewahakikishia wafugaji wa samaki kwa vizimba nchini kuwa Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha upatikanaji wa chakula cha samaki na vifaa muhimu vya ufugaji unaboreshwa ili kukuza tija katika sekta hiyo inayokua kwa kasi nchini.

Kauli hiyo imetolewa leo Mei 26, 2026 bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Dkt. Bashiru Ali, wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Bunda Mjini, Ester Bulaya (CCM), aliyehoji kuhusu changamoto ya upatikanaji wa chakula cha samaki kwa wafugaji wa vizimba pamoja na mpango wa Serikali wa kuwapatia boti za kisasa wafugaji wa Wilaya ya Bunda.

Akijibu swali hilo, Dkt. Bashiru amesema Serikali inatambua uwepo wa changamoto ya upungufu wa chakula cha samaki, hasa kutokana na kuongezeka kwa kasi kwa shughuli za ufugaji wa samaki kwa vizimba katika maeneo mbalimbali nchini.

Amesema ufugaji wa samaki kwa vizimba ni moja ya sekta mpya zinazokua kwa kasi kubwa na zimeendelea kuvutia wawekezaji pamoja na wananchi wengi wanaotafuta fursa za kiuchumi kupitia sekta ya uvuvi na ufugaji wa samaki.

“Kadri shughuli hizi zinavyopanuka, mahitaji ya chakula cha samaki nayo yanaongezeka kwa kiwango kikubwa, jambo ambalo kwa kipindi fulani limekuwa likisababisha changamoto ya upatikanaji wa chakula hicho kwa wakati,” amesema Dkt. Bashiru.

Hata hivyo, Waziri huyo amesema hali hiyo inaanza kuimarika kutokana na kuongezeka kwa uwekezaji katika viwanda vya uzalishaji wa chakula cha samaki nchini.

Amevitaja baadhi ya viwanda hivyo kuwa ni pamoja na kiwanda kilichopo Dar es Salaam pamoja na viwanda vingine vilivyoanzishwa jijini Mwanza na katika maeneo mengine kupitia wawekezaji binafsi waliovutiwa na mahitaji makubwa ya soko.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, kuongezeka kwa wazalishaji wa chakula cha samaki kutasaidia kushusha bei ya bidhaa hiyo na hivyo kupunguza gharama kwa wafugaji wa samaki nchini.

“Kadri wazalishaji wa chakula cha samaki wanavyoongezeka, ushindani unaongezeka na bei zinaendelea kushuka, jambo ambalo litasaidia kufanya shughuli za ufugaji wa samaki kuwa nafuu zaidi kwa wananchi,” amesema.

Aidha, Dkt. Bashiru amesema Serikali inaendelea kuweka mazingira rafiki kwa wawekezaji wa sekta hiyo ili kuhakikisha uzalishaji wa chakula cha samaki unaongezeka sambamba na mahitaji yaliyopo sokoni.

Amefafanua kuwa gharama za chakula cha samaki ndizo zinazobeba sehemu kubwa ya matumizi katika ufugaji wa samaki kwa vizimba, ambapo zaidi ya asilimia 70 ya gharama zote za uzalishaji hutokana na ununuzi wa chakula hicho.

Kutokana na hali hiyo, amesema Serikali inalenga kuhakikisha upatikanaji wa chakula hicho unakuwa wa uhakika na kwa bei nafuu ili kuongeza faida kwa wafugaji na kuvutia wananchi wengi zaidi kuingia kwenye sekta hiyo.

Kuhusu suala la upatikanaji wa boti za kisasa kwa wafugaji wa samaki kwa vizimba wilayani Bunda, Waziri huyo amesema Serikali tayari imeunda tume maalumu yenye jukumu la kupitia na kuboresha mfumo wa utoaji wa boti hizo.

Amesema lengo la hatua hiyo ni kuhakikisha boti zitakazotolewa zinakidhi viwango vinavyotakiwa na mahitaji halisi ya wafugaji ili ziweze kusaidia shughuli za ufugaji kwa ufanisi zaidi.

Dkt. Bashiru ameongeza kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa sekta ya uvuvi na ufugaji wa samaki ili kuimarisha uchumi wa wananchi kupitia sekta hiyo ambayo imeendelea kuonekana kuwa na mchango mkubwa katika ajira, lishe na ukuaji wa uchumi wa Taifa.




MBUNGE wa Viti Maalum Mkoa wa Pwani, Mariam Ibrahim amemshukuru Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM)Taifa , Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kwa kupendekeza jina lake na Kamati Kuu ya chama hicho kulipitisha na hatimaye kushinda kwa kura nyingi.
Ametoa shukrani hizo kwa Mwenyekiti wa CCM Taifa ,Rais Dk.Samia Suluhu Hassan alipokuwa akisalimia viongozi mbalimbali wa Chama hicho wakati wa semina ya Uongozi na Maendeleo kwa Madiwani wote wanawake  wa Mkoa wa Pwani.

“Nitumie nafasi hii kwa dhati ya moyo wangu kumshukuru Mwenyekiti wetu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM)Taifa Dk.Samia Suluhu Hassan kwa kunipendekeza mimi na Kamati Kuu kurudisha jina langu na kuja katika Mkoa wa Pwani na kupigiwa kura nyingi.

“Waheshimiwa madiwani hatujaonana toka Uchaguzi mkuu ulivyopita hivyo naomba kuchukua fursa hii kuwashukuru nyote kwa kura zenu za kishindo.Nasema ahsanteni sana,amesema mbele ya madiwani hao pamoja na viongozi wa Mkoa huo.

Amesisitiza ameamua kutoa shukrani hizo kwasababu ndio mara yake ya kwanza wanakutana ambapo ametumia nafasi hiyo pia kuwaaahidi kuendelea kushirikiana nao na yupo tayari kwa wakati wowote ambao atahitahika.“Tutakuwa pamoja katika kila hali.”







 




- Serikali yapunguza gharama za leseni ya Madini Chumvi, wachimbaji wanufaika


📍Mtwara


Mkoa wa Mtwara umeendelea kujidhihirisha kuwa kitovu muhimu cha uwekezaji katika sekta ya chumvi kutokana na uwepo wa fukwe zinazofaa kwa uzalishaji, maboresho ya mazingira ya biashara na ongezeko la uzalishaji linalofikia takribani tani 90 kwa majaruba manne katika baadhi ya maeneo ya uzalishaji.

Kutokana na hatua hiyo, wachimbaji na wazalishaji wa chumvi wameanza kunufaika na fursa mpya za kiuchumi kupitia kuongezeka kwa uzalishaji, ajira na upanuzi wa maeneo ya uzalishaji.

Akizungumza katika mahojiano maalum, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Mtwara, Winnifrida Mrema, amesema sekta ya chumvi mkoani humo inaendelea kukua kwa kasi kutokana na kuimarika kwa shughuli za uzalishaji pamoja na matumizi ya teknolojia za kisasa katika uchakataji wa chumvi.

Amesema maboresho hayo yanalenga kuongeza ubora wa chumvi kwa matumizi ya majumbani, viwandani na mifugo, huku yakichochea ajira kwa wananchi wa maeneo yanayozunguka mashamba ya chumvi.

“Mtwara ina mazingira rafiki kwa uzalishaji wa chumvi na Serikali inaendelea kuhamasisha uwekezaji katika sekta hii ili kuongeza mapato kwa wananchi na taifa kwa ujumla,” amesema Mrema.

Katika Kijiji cha Mnete, Kata ya Nalingu Halmashauri ya Mtwara Vijijini, msimamizi wa mashamba ya chumvi, Salum Amani, amesema mashamba hayo yanamilikiwa na Zamda Khatibu na yana leseni mbili za uvunaji chumvi pamoja na majaruba 24 yanayotumika kwa uzalishaji.

Amesema kwa sasa wanaendelea na shughuli za usafishaji wa majaruba baada ya msimu wa mvua ili kuruhusu maji ya chumvi kuingia tayari kwa uzalishaji mpya.

Kwa mujibu wa Salum, uzalishaji wa chumvi hutegemea hali ya hewa, ambapo jua kali huwezesha chumvi kukauka ndani ya siku 30, huku hali ya baridi ikifanya mchakato huo kuchukua hadi siku 40.

“Kwa kawaida majaruba manne huzalisha takribani tani 90 za chumvi kwa msimu mmoja, huku shughuli hizi zikitoa ajira kwa wafanyakazi tisa katika eneo hili,” amesema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Wazalishaji Chumvi Mkoa wa Mtwara na Mwenyekiti wa Kamati ya Chumvi kupitia FEMATA, Khalfan Nassoro, amesema kupunguzwa kwa gharama ya ada ya pango ya leseni za chumvi kutoka Shilingi 45,000 hadi Shilingi 20,000 kumeongeza uwezo wa wazalishaji kupanua maeneo ya uzalishaji.

Amesema hatua hiyo imeongeza matumaini kwa wawekezaji na wachimbaji wadogo, huku akisisitiza kuwa mazingira bora ya uwekezaji yataifanya Mtwara kuwa kitovu kikuu cha uzalishaji wa chumvi nchini.

Nassoro amesema pia ukuaji wa sekta hiyo unaweza kuchochea ujenzi wa viwanda vya kuongeza thamani ya chumvi na hivyo kuongeza mchango wa sekta hiyo katika uchumi wa taifa.




Na Janeth Raphael MichuziTv Bungeni - Dodoma


Serikali imesema ipo katika hatua za mwisho za kukamilisha uhakiki wa madeni ya waliokuwa wafanyakazi wa Mgodi wa Kiwira kabla ya kuanza mchakato wa malipo ya madai yao yaliyodumu kwa miaka kadhaa.

Kauli hiyo imetolewa bungeni leo na Naibu Waziri wa Madini Dkt Steven Kiruswa wakati akijibu swali la Mbunge wa Kyela, Baraka Ulimboka Mwamengo, ambaye alihoji ni lini Serikali itawalipa waliokuwa watumishi wa mgodi huo.

Akijibu swali hilo, Dkt Kiruswa amesema deni la wafanyakazi wa Kiwira lilitokana na malalamiko ya mapunjo ya mafao kwa wafanyakazi waliokuwa wakihudumu katika mgodi huo kabla ya kubinafsishwa.

Ameeleza kuwa baada ya malalamiko hayo kuwasilishwa na Chama cha Wafanyakazi Migodini na Ujenzi (TAMICO), Serikali kupitia Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ilifanya ukaguzi maalum mwezi Novemba mwaka 2008 ili kuchunguza madai hayo.

Aidha, amesema kuwa baadaye iliyokuwa Wizara ya Nishati na Madini iliunda timu maalum iliyofanya uhakiki mwingine wa madeni hayo mwezi Desemba mwaka 2015 kwa lengo la kubaini kiwango halisi cha madai ya wafanyakazi hao.

Dkt Kiruswa amesema matokeo ya uhakiki yalionesha kuwa madai halali ya wafanyakazi yalifikia shilingi bilioni 1.024 kwa wafanyakazi 893, tofauti na madai ya awali ya shilingi bilioni 47 yaliyokuwa yakidaiwa na watumishi 1,687.

Mbali na madai ya wafanyakazi, Serikali pia ilibaini uwepo wa madeni ya wazabuni mbalimbali, ikiwemo kampuni iliyokuwa ikitoa huduma za ulinzi katika mgodi huo, yenye madai ya takribani shilingi milioni 496.

Amesema jumla ya madeni yote yaliyohakikiwa ilifikia shilingi bilioni 1.52, ambazo ziliingizwa rasmi katika orodha ya madeni ya Serikali kwa ajili ya kushughulikiwa.

Amebainisha kuwa Wizara ya Madini inaendelea kushirikiana na Wizara ya Fedha kuhakikisha malipo hayo yanafanyika mara baada ya kukamilika kwa hatua zote muhimu za uhakiki.

Aidha, amefafanua kuwa mwaka 2025 Wizara ya Fedha ilituma timu ya wataalamu kufanya uhakiki mwingine wa mwisho ili kujiridhisha na taarifa iliyotolewa katika uhakiki wa mwaka 2015 kabla ya Serikali kuanza kulipa madai hayo.

“Kwa sasa timu ya wataalamu inakamilisha taarifa ya mwisho ya uhakiki ili kuwezesha Serikali kuanza mchakato wa kulipa madeni hayo,” alisema Waziri huyo.

Hatua hiyo imeendelea kuibua matumaini kwa mamia ya waliokuwa wafanyakazi wa Mgodi wa Kiwira ambao wamekuwa wakisubiri kwa muda mrefu kupatiwa haki zao baada ya madai yao kuchelewa kushughulikiwa kwa miaka mingi.



Benki ya Absa Tanzania imezindua rasmi suluhisho bunifu la mikopo ya muda mfupi inayolenga kuwawezesha wafanyabiashara wadogo na wa kati kukuza biashara zao bila hitaji la dhamana.

Huduma hiyo mpya imeundwa mahsusi kwa wafanyabiashara wanaojihusisha na biashara ya bidhaa na huduma, wakiwemo wauzaji wa jumla, wasambazaji, mawakala na wauzaji wa rejareja wanaotumia mashine za malipo zinazotolewa na benki hiyo, Absa Point-of-Sale (POS) pamoja na njia nyingine za kidijitali za malipo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo jijini Dar es Salaam, Mkuu wa Kitengo cha Bidhaa na Njia za Malipo wa Benki ya Absa Tanzania, Jane Kalumuna, alisema huduma hiyo inalenga kuondoa changamoto kubwa inayowakabili wafanyabiashara wengi ya kushindwa kupata mikopo kutokana na kukosa dhamana za kawaida.

Alisema wafanyabiashara wengi wamekuwa wakifanya mauzo ya kila siku yenye mtiririko mzuri wa fedha, lakini bado wamekuwa wakikosa fursa za kupata mikopo kwa sababu mifumo mingi ya kifedha hutegemea zaidi dhamana kuliko uwezo halisi wa biashara.

“Kwa muda mrefu, biashara nyingi zenye mtiririko mzuri wa fedha zimekuwa zikikosa huduma za kifedha kwa sababu hazina dhamana za kawaida. Kupitia Absa huduma hii, tunabadilisha simulizi hilo kwa kutambua na kuthamini utendaji halisi wa biashara,” alisema Bi. Jane.

Aliongeza kuwa huduma hiyo inatumia historia ya miamala ya POS kupima uwezo wa mfanyabiashara kukopa, hivyo kuwezesha wafanyabiashara kupata fedha kwa haraka kulingana na mwenendo halisi wa biashara zao.

Naye Meneja Masoko na Mawasiliano na Chapa wa Benki ya Absa Tanzania, Beda Biswalo, alisema huduma hiyo ni sehemu ya dhamira ya benki hiyo ya kuwezesha ukuaji wa biashara na uchumi wa Tanzania kwa ujumla.

“Kwa kuondoa kikwazo cha dhamana na kubadilisha mauzo ya kila siku kupitia POS kuwa chanzo cha haraka cha mtaji, tunabadilisha namna biashara zinavyopata huduma za kifedha nchini Tanzania. Tunaamini kuwa kila mfanyabiashara ana simulizi muhimu, na suluhisho hili linaakisi ahadi yetu ya kusikiliza na kusaidia ukuaji wao,” alisema Biswalo.

Aliongeza kuwa kupitia huduma hiyo, Absa inaendeleza dhamira yake ya ‘Kuiwezesha Afrika ya Kesho Pamoja, Hatua Moja baada ya Nyingine’ kwa kusaidia biashara kukua, kupanuka na kuchangia maendeleo ya uchumi wa taifa.

Huduma ya Absa Merchant Financing inatarajiwa kusaidia kuziba pengo la upatikanaji wa mikopo kwa wafanyabiashara wengi nchini huku ikiimarisha ujumuishaji wa kifedha na mahusiano ya muda mrefu kati ya benki na wateja wake.


 Mkuu wa Kitengo cha Bidhaa na Njia za Malipo wa Benki ya Absa Tanzania, Jane Kalumuna (wa tatu kushoto) na wengine kutoka kushoto; Meneja Masoko, Mawasiliano na Chapa, Beda Biswalo, Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Wateja Wadogo na wa Kati, Scolastica Dominic na Meneja Mauzo wa Kitengo cha machine za malipo (POS), Edward Edwine, wakionesha mashine hizo kama ishara ya uzinduzi rasmi wa huduma ya mikopo isiyo na dhamana yenye lengo la kukuza biashara za wafanyabiashara wadogo na wa kati wanaofanya mauzo kwa kutumia POS za Absa. Hafla hiyo ilifanyika jijini Dar es Salaam leo.


Mkuu wa Kitengo cha Bidhaa na Njia za Malipo wa Benki ya Absa Tanzania, Jane Kalumuna (wa tatu kushoto) na wengine kutoka kushoto; Meneja Masoko, Mawasiliano na Chapa, Beda Biswalo, Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Wateja Wadogo na wa Kati, Scolastica Dominic na Meneja Mauzo wa Kitengo cha machine za manunuzi (POS), Edward Edwine, wakiwa katika mkutano na waandishi wa habari, jijini Dar es leo, katika hafla ya uzinduzi rasmi wa huduma ya mikopo isiyo na dhamana yenye lengo la kukuza biashara za wafanyabiashara wadogo na wa kati wanaofanya mauzo kwa kutumia POS za Absa.
Mkuu wa Kitengo cha Bidhaa na Njia za Malipo wa Benki ya Absa Tanzania, Jane Kalumuna (wa tatu kushoto, waliokaa) na wengine kutoka kushoto; Meneja Masoko, Mawasiliano na Chapa, Beda Biswalo, Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Wateja Wadogo na wa Kati, Scolastica Dominic na Meneja Mauzo wa Kitengo cha machine za manunuzi (POS), Edward Edwine, wakionesha mashine hizo kama ishara ya uzinduzi rasmi wa huduma ya mikopo isiyo na dhamana yenye lengo la kukuza biashara za wafanyabiashara wadogo na wa kati wanaofanya mauzo kwa kutumia POS za Absa. Hafla hiyo ilifanyika jijini Dar es Salaam leo. Wengine ni baadhi ya wafanyakazi wa kitengo cha biashara.




Vodacom M-Pesa Tanzania imetangaza ushirikiano mpya na PayPal ambao utawezesha wateja nchini Tanzania kufanya miamala kwa urahisi kati ya akaunti zao za PayPal na pochi za M-Pesa kupitia M-Pesa Super App. Kama sehemu ya suluhisho pana la malipo ya kimataifa la M-Pesa, hatua hii inaashiria maendeleo muhimu katika kupanua upatikanaji wa huduma za kifedha za kidijitali za kimataifa.

Kupitia mfumo huu mpya, wateja wa M-Pesa watakaokidhi vigezo wataweza kuweka fedha moja kwa moja kwenye akaunti zao za PayPal na pia kutoa fedha kutoka PayPal kwenda kwenye akaunti zao za M-Pesa kwa njia salama na rahisi zaidiHuduma hii inaenda kurahisisha miamala ya kimataifa kwa wafanyakazi wa kujitegemea (freelancers), watengeneza maudhui, wajisiriamali wanaoshiriki uchumi wa kazi za muda (gig economy), pamoja na Watanzania wengine waliounganishwa kidijitali.

Ushirikiano huu unakuja wakati mahitaji ya huduma rahisi za malipo ya kuvuka mipaka yanaendelea kuongezeka miongoni mwa Watanzania wanaoshiriki katika biashara za kimataifa, kazi za kujitegemea na huduma za kidijitali. Kupitia huduma hii ya kuwezesha utoaji wa fedha kutoka PayPal kwenda M-Pesa, Watanzania sasa wataweza kupata na kutumia mapato yao ya PayPal kwa urahisi zaidi.

Akizungumza kuhusu ushirikiano huo, Kaimu Mkurugenzi wa M-Pesa, Tulisindo Mlupilo, alisema ushirikiano huo unaonesha dhamira endelevu ya M-Pesa ya kuwaunganisha wateja na fursa zaidi kupitia ubunifu na huduma jumuishi za kifedha.

“Uunganisho wa kidijitali unaendelea kufungua fursa nyingi zaidi kwa Watanzania kushiriki katika uchumi wa kimataifa kupitia biashara za mtandaoni, kazi za kujitegemea, utengenezaji wa maudhui na biashara za kuvuka mipaka. Kupitia ushirikiano huu na PayPal, tunawarahisishia zaidi wateja wetu kutuma, kupokea, na kutoa fedha kati ya mifumo hii kwa urahisi na uhakika zaidi,” alisema Mlupilo.

Otto Williams, Makamu wa Rais Mwandamizi, Mkuu wa Kanda na Meneja Mkuu wa Mashariki ya Kati na Afrika wa PayPal, alisema ushirikiano huo unawezesha muingiliano mkubwa zaidi wa mifumo kwa wateja wanaofanya miamala ya kidijitali ya kimataifa

“Duniani kote, tunaendelea kushuhudia ukuaji wa biashara za kidijitali pamoja na ongezeko la ushiriki wa watu katika kazi za mtandaoni. Kwa kuwezesha uhamishaji rahisi wa fedha kati ya PayPal na M-Pesa kupitia kuunganisha akaunti, ushirikiano huu utasaidia kutoa huduma ya malipo ya kuvuka mipaka iliyo rahisi, salama na yenye ufanisi zaidi kwa wateja nchini Tanzania,” alisema Williams.

Wateja wataweza kutumia huduma hiyo moja kwa moja kupitia M-Pesa Super App kwa kuunganisha akaunti zao za PayPal na akaunti zao za M-Pesa kupitia mfumo rahisi wa usajili na uthibitishaji utakaowezesha miamala salama na rahisi kati ya mifumo hiyo miwili.

Ushirikiano huu unaendelea kuimarisha nafasi ya M-Pesa kama kinara wa huduma za kifedha za kidijitali na ubunifu nchini Tanzania, huku ukiunga mkono juhudi pana za kukuza ujumuishaji wa kifedha na kuongeza ushiriki wa Watanzania katika uchumi wa kidijitali.

Maelezo zaidi kuhusu namna ya kujiunga na huduma hii, viwango vya miamala, muda wa kuanza kwa huduma pamoja na mwongozo wa matumizi yatatolewa kupitia:tovuti rasmi ya Vodacom Tanzania na njia nyingine rasmi za mawasiliano za M-Pesa.



Top News