Na Munir Shemweta, WANMM Nairobi

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt Leonard Akwilapo, amekutana na kufanya mazungumzo na Afisa Mtendaji Mkuu wa Shelter Afrique Bw. Thierno-Habib Hann jijini Nairobi, nchini Kenya.

Viongozi hao wawili wamekutana pembezoni mwa Kongamano la Miji Afrika (2nd Africa Urban Forum) lililofanyika kuanzia Aprili 8 hadi 10, 2026 nchini Kenya, na kukutanisha mataifa mbalimbali Barani Afrika kwa lengo la kubadilishana uzoefu na suluhisho bunifu katika kukabiliana na changamoto za maendeleo ya miji na makazi.

Dkt Akwilapo na Bw.Thierno-Habib Hann katika kikao chao walijadili masuala mbambali yanayohusu uimarishaji wa upatikanaji wa makazi nafuu kwa wananchi pamoja na ushirikiano kati ya serikali na taasisi za kifedha katika kufanikisha azma hiyo.

Shelter Afrique ni taasisi ya kifedha ya kimataifa inayolenga kusaidia maendeleo ya makazi Barani Afrika, huku makao makuu yake makuu yakiwa jijini Nairobi nchini Kenya.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (Kulia) akizungumza na Mtendaji Mkuu wa Shelter Afrique Bw.Thierno-Habib Hann jijini Nairobi, Kenya walipokutana pembezoni mwa Kongamano la pili la Miji Afrika (2ND Africa Urban Forum) lilofanyika nchini humo.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (Kushoto) na Mtendaji Mkuu wa Shelter Afrique Bw.Thierno-Habib Hann wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kikao chao jijini Nairobi, Kenya, walipokutana pembezoni mwa Kongamano la pili la Miji Afrika lilofanyika nchini humo.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (Kulia) akitambulishwa baadhi ya maafisa wa taasisi ya Shelter Afrique alipokutana na Mtendaji Mkuu wa taasisi hiyo Bw.Thierno-Habib Hann pembezoni mwa Kongamano la pili la Miji Afrika (2nd Africa Urban Forum) lilofanyika jijini Nairobi nchini Kenya. (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)

 



Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar,  Alhaj Hemed Suleiman Abdulla ametoa maelekezo kwa Taasisi zinazohusika na uratibu wa Ibada ya Hijja kwa mwaka 2026, kufanya mageuzi ya kimfumo ili kuboresha utoaji wa huduma kwa Mahujaji 4,029 kutoka Tanzania. 


Mhe. Abdullah amesema hayo katika Kikao kilichofanyika Visiwani Zanzibar leo ambapo amesisitiza umuhimu wa kuachana na mifumo ya kizamani na badala yake kuimarisha matumizi ya mifumo ya kidijitali.

Aidha, ameelekeza kuanzishwa kwa mfumo wa Kanzidata (database) utakaokuwa na taarifa sahihi za Mahujaji hao ili kurahisisha mipango na utoaji wa huduma.

Pia, amesisitiza umuhimu wa Taasisi hizo kuzingatia maslahi ya taifa kwa kuepuka migongano ya kimaslahi na kuhakikisha huduma zinatolewa kwa usawa. Ameeleza kuwa maelekezo hayo yanapaswa kuanza kutekelezwa mara moja ili kuhakikisha maandalizi ya msimu wa Hijja 2026 yanafanyika kwa ufanisi ili kuimarisha taswira ya nchi kimataifa.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Ayoub Mohammed Mahmoud amesema kuwa Wizara imeendelea kusaidia uratibu wa Hijja kupitia kitengo chake cha Usajili wa Jumuiya na imefanikisha upatikanaji wa hati za kusafiria kwa Mahujaji hao, kwa ufanisi mkubwa ili kuhakikisha zoezi hilo la Maandalizi ya Ibada linafanyika kwa ukamilifu

Naye, Waziri wa Kazi, Ajira na Mahusiano, Deus Sangu amesema Idadi ya Mahujaji imeendelea kuongezeka, kutokana na ongezeko hilo kumekuwa na changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika maandalizi na uratibu wa safari hizo. Hivyo, Serikali imeanza kufuatilia maandalizi hayo kwa lengo la kuweka miongozo bora itakayosaidia kuhakikisha wanapata huduma na maelekezo sahihi wanapoelekea kutekeleza Ibada hiyo.


 

Zaidi ya Watalii 90 wametembela Hifadhi ya Taifa Mkomazi kuvinjari na kufurahia utalii wa ndani leo Aprili 11, 2026 kufuatia ufunguzi wa tamasha la utalii lijulikanalo kama Same Utalii Festival msimu wa Tatu katika viwanja vya stendi wilayani Same, Mkoani Kilimanjaro.

Watalii hao walipata fursa ya kutembelea maeneo mbalimbali ya hifadhi ikiwemo Mbula, Kisima na Njiro na kujionea wanyamapori aina ya faru weusi, kivutio kinachowavutia wazawa na wageni lukuki toka nje na ndani ya mipaka ya Same kushuhudia ikolojia ya wanyama hao.

Akizindua rasmi tamasha hilo Waziri Mkuu (Mst.) wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyelitumikia Taifa kwa kipindi cha Awamu ya Nne kati ya mwaka 1990 hadi 1994 Mhe. John Malecela alisema kuwa matamasha haya ni kichocheo kikubwa cha utalii na hifadhi pia zina nafasi kubwa ya kuibua mazao mapya ya utalii yatakayochagiza kuongeza idadi ya watalii  kutembelea hii kwa kuwa na vionyo tofauti.

Aidha, Mhe. Malecela aliongeza kuwa utalii wetu uanze na sisi watanzania wenyewe ndani ya vivutio vyetu na hii ni kutokana na gharama nafuu zilizowekwa pamoja na uwezo mkubwa wa kufikia maeneo hayo kwa wepesi tofauti na wale wanaotoka maeneo ya mbali.

Naye, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii Mhe. John Mabula alieleza kuwa idadi ya watalii katika Hifadhi ya Taifa Mkomazi imeongeza kwa kiasi kikubwa kutoka 7800 kwa mwaka na kufikia 11000 kwa mwaka 2022 hadi 2026. Kadhalika alieleza kuwa uwepo wa vivutio na ongezeko la wageni ni fursa kwa wazawa kuweza kujiinua kibiashara na kuongeza kipato katika kaya zao.

Kwa, upande wake Mkuu Wilaya ya Same Mhe. Kasilda Mgeni alieleza kuwa Hifadhi ya Taifa Mkomazi iwape fursa vijana wa bodaboda kwa kutoa elimu ya kuongoza wageni ili wanapowapokea watalii waweze kuwakaribisha na kuwapa miongozo ya awali itakayochangia pato katika majukumu yao.

Hifadhi ya Taifa Mkomazi imekuwa moja ya kivutio pendwa katika  tamasha hili kwa kuwakutanisha wageni mbalimbali kutoka nje na ndani ya wilaya ya Same kutembelea wanyamapori adimu ikiwemo faru weusi, mbwa mwitu pamoja na uoto wa asili unaoipamba hifadhi hiyo. 













 



Na Oscar Assenga, Tanga

Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Tanga kimeeleza kuwa suluhisho la kudumu la kuboresha eneo la kuchezea katika Uwanja wa CCM Mkwakwani ni uwekaji wa nyasi bandia, huku wakipanga kushirikiana na wadau wa soka kufanikisha mpango huo.

Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua uwanja huo, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga, Rajab Abdurahman, alisema uwekaji wa nyasi bandia unakadiriwa kugharimu kati ya shilingi milioni 400 hadi 500.

Ziara hiyo ni sehemu ya ukaguzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo mkoani humo, ikiwemo ile inayotekelezwa kwa fedha zinazotolewa na Serikali chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa lengo la kupunguza kero kwa wananchi.

Abdurahman aliwataka viongozi wa CCM, ambao ni wamiliki wa uwanja huo, kutumia ubunifu na kushirikiana na wadau wa soka ili kuhakikisha wanapata fedha za kuweka nyasi bandia.

“Tutawaomba wadau wa soka nchini watakapohitajika kutusaidia, kwani dhamira yetu ni njema. Kama ambavyo wamekuwa wakitusaidia hapo awali, tunaamini watashiriki nasi kuhakikisha tunakuwa na uwanja wa kisasa zaidi,” alisema.

Alieleza kuwa maboresho ya uwanja huo yatasaidia kuinua uchumi wa Mkoa wa Tanga, kwani utaweza kutumika kwa mashindano ya kitaifa na kimataifa, ikiwemo CECAFA na michuano mingine ya Afrika.

“Tunapokuwa na uwanja mzuri, hata timu za nje zitakuja kucheza hapa Tanga. Hii itaongeza mzunguko wa fedha na kukuza uchumi wa mkoa wetu,” aliongeza.

Aidha, alikumbusha kuwa uwanja huo uliwahi kufungiwa kutokana na kutokidhi vigezo, hasa ubora wa eneo la kuchezea, akisisitiza kuwa hatua zinazochukuliwa sasa zinalenga kuhakikisha viwango vinazingatiwa kwa usalama wa wachezaji na ubora wa mchezo.

“Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) linapofungia uwanja si kwa kupenda, bali kuhakikisha viwango vinazingatiwa. Ndiyo maana tumekuwa wepesi kuchukua hatua za maboresho,” alisema.

Katika hatua nyingine, Abdurahman alieleza kuridhishwa na maendeleo ya ufungaji wa viti 6,500 vilivyotolewa na TFF chini ya Rais wake, Wallace Karia, licha ya kuwepo kwa ucheleweshaji mwanzoni.

Amesema tayari ameagiza kazi hiyo ikamilike ndani ya mwezi mmoja, na kwa sasa inaendelea vizuri chini ya usimamizi wa Mjumbe wa Kamati ya Siasa ya Mkoa, Nasoro Makau.

Kwa mujibu wa mpango huo, maeneo ya kipaumbele ni jukwaa kuu pamoja na sehemu za mashabiki wa klabu za Coastal Union na African Sports. Pia wameomba viti vingine 2,500 ili kukamilisha uwanja mzima.

Abdurahman aliishukuru Serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, inayoongozwa na Waziri Paul Makonda na Naibu wake Hamisi Mwinjuma, pamoja na Rais wa TFF Wallace Karia, kwa ushirikiano wao katika kuboresha uwanja huo.

Alisisitiza kuwa maboresho hayo yanalenga kuhakikisha klabu za Coastal Union na African Sports zinaendelea kucheza mechi zao za nyumbani mkoani Tanga badala ya kuhamishiwa maeneo mengine.

Aidha, aliwataka mashabiki wa soka kujitokeza kwa wingi uwanjani kuunga mkono timu zao.

“Haileti maana kuwa na uwanja mzuri halafu mashabiki wanabaki nyumbani kuangalia mechi,” alisisitiza.

Kwa upande wake, Meneja wa Uwanja wa Mkwakwani, Nasoro Makau, alisema hadi sasa wamefikia asilimia 40 ya ufungaji wa viti na wana uhakika wa kukamilisha kazi hiyo ndani ya mwezi mmoja.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ametoa wito kwa vijana kusimama imara na kulinda umoja, kujenga uadilifu, kutumia elimu na ubunifu katika kukuza maendeleo ya nchi ili kuweza kumuenzi Baba wa Taifa Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere kwa vitendo.

Makamu wa Rais ametoa wito huo wakati akifungua Kongamano la Vijana katika Kumbukizi ya Miaka 104 ya Kuzaliwaa Baba wa Taifa, Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere, lililofanyika Ukumbi wa Chimwaga mkoani Dodoma, leo tarehe 11 Aprili 2026. Amesema ni muhimu kwa vijana kutambua wajibu wa msingi wa kizazi hiki, kwa kuhakakikisha wanafanya kila jitihada kuimarisha misingi ya kujitegemea kiuchumi, kiakili na kimaamuzi ili kuijenga nchi.

 Makamu wa Rais amesema Hayati Baba wa Taifa alikuwa kiongozi aliyeunganisha Taifa na kutoa mchango mkubwa katika ukombozi wa Bara la Afrika. Amesema Taifa la Tanzania lilipata bahati ya pekee kuwa na Hayati Mwl. Nyerere kwa kuwa alichukia rushwa, ubadhirifu na matumizi mabaya ya madaraka. Aliamini katika utu na uhuru wa mwanadamu ikiwemo msisitizo wa kuhakikisha kila wananchi anapata elimu.

Ameongeza kwamba Baba wa Taifa alitengeneza misingi ya amani, utulivu na mshikamano katika Taifa pamoja na kufundisha vitu vyote vinavyoweza kuleta mpasuko kama vile ukabila, dini, rangi, kupuuza maendeleo na usawa katika jamii.

Makamu wa Rais amesema ni dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kuendeleza mshikamano na umoja ambao Baba wa Taifa aliujenga.

 Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi wa Taasisi ya Kumbukumbu ya Mwal. Nyerere ambaye ni Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Mizengo Pinda ametoa rai kwa vijana kuhakikisha wanafanya jitihada za kujifunza historia ya Taifa ili kufahamu waliotoa mchango mkubwa katika historia hiyo.

Amewahimiza kusoma vitabu vilivyoandikwa kuhusu Hayati Mwal.Julius Kambarage Nyerere ili kufahamu mchango mkubwa aliyoutoa katika ukombozi wa Bara la Afrika na msisitizo alioutoa wa katika kuhakikisha umoja wa Afrika. Ameongeza Taasisi hiyo imejikita katika kutoa mchango kwa kuwasaidia viongozi vijana kuwa wazalendo na wanaowajibika.

 Kongamano hilo limejadili mada mbalimbali zenye lengo la kuwajengea vijana uzalendo, uwajibikaji, matumizi sahihi ya mitandao na matumizi bora ya fursa zilizopo nchini.






Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, tarehe 11 Aprili, 2026 akiwa Ikulu, Dodoma, amezungumza kwa njia ya mtandao na Chuo Kikuu cha Jimbo la Nasarawa, Keffi nchini Nigeria, kufuatia kutunukiwa Shahada ya Uzamivu ya Heshima kwa kutambua mchango wake katika maendeleo ya Bara la Afrika.

Katika hotuba yake, Rais Samia alieleza mshangao wake alipopokea taarifa ya tuzo hiyo kupitia barua kutoka kwa Mheshimiwa Abdullah Isule, Gavana wa Jimbo la Nasarawa. Alisema kilichomgusa zaidi ni kutambuliwa kwa mchango wake katika maendeleo ya Afrika, akibainisha kuwa anapokea heshima hiyo kwa unyenyekevu mkubwa na shukrani.

Amesisitiza kuwa tuzo hiyo si yake binafsi, bali ni ishara ya juhudi za pamoja za Watanzania na matarajio yao ya maendeleo, ushirikiano na ustawi wa binadamu.

Akielezea historia yake, Rais Samia alisema ametoka katika familia ya kawaida na kulelewa katika mazingira ya kijijini yaliyojengwa katika misingi ya unyenyekevu, bidii na maadili ya kijamii. Aliongeza kuwa elimu yake ya awali Zanzibar ilimfungulia macho kuhusu changamoto zinazowakabili wasichana wengi, ikiwemo ukosefu wa rasilimali na mitazamo hasi ya kijamii inayowazuia wanawake kushiriki kikamilifu katika maendeleo.

Amesema uzoefu huo ulimjengea azma ya kupambana na vikwazo hivyo si kwa manufaa yake binafsi pekee, bali kwa ajili ya wanawake na wasichana wengine.

Katika safari yake ya uongozi na utumishi wa umma, Rais Samia amejikita katika kuwawezesha wanawake na wasichana kwa kuhamasisha ushiriki wao katika uongozi, elimu na shughuli za kiuchumi. Alisisitiza kuwa hakuna jamii inayoweza kufikia maendeleo ya kweli ikiwa itawaacha nyuma wanawake, ambao ni sehemu kubwa ya jamii.

Aidha, Rais Samia amesema kuwa juhudi zake katika ustawi wa wanawake na watoto zimechangia kuteuliwa kwake na Umoja wa Afrika kuwa kinara wa afya ya mama na mtoto. Pia amewahi kuwa kinara wa biashara huru ya Afrika kwa wanawake na vijana, pamoja na kinara wa nishati safi ya kupikia barani Afrika.

Hotuba yake ilihitimishwa kwa kusisitiza umuhimu wa kuendeleza mshikamano na ushirikiano miongoni mwa mataifa ya Afrika ili kufanikisha maendeleo endelevu na ustawi wa watu wake.


Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma .

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ametoa wito kwa wanawake na vijana barani Afrika kuongeza juhudi, kujituma na kujiamini katika ndoto zao ili kufanikisha maendeleo ya binafsi na ya kijamii.

Rais Samia ametoa kauli hiyo leo Aprili 11, 2026, mara baada ya kutunukiwa shahada ya heshima na Chuo Kikuu cha Nasarawa, tukio ambalo limebeba heshima kubwa kwa uongozi wake na mchango wake katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Akizungumza baada ya tukio hilo, Rais Samia amesema safari yake ya uongozi ni ushahidi tosha kwamba mafanikio yanawezekana hata pale mtu anapokutana na changamoto mbalimbali za maisha, mradi tu awe na bidii, ujasiri na maono ya mbali.

Amebainisha kuwa Serikali na yeye binafsi wamekuwa mstari wa mbele katika kuhamasisha ushiriki wa wanawake katika nafasi za uongozi, elimu na sekta ya uchumi, akisisitiza kuwa hakuna jamii inayoweza kufikia maendeleo kamili iwapo nusu ya nguvu kazi (wanawake) haitashirikishwa kikamilifu.

Aidha, amewahimiza wahitimu kutumia elimu waliyoipata kama chachu ya mabadiliko chanya katika jamii zao, kwa kuanzisha miradi, kubuni suluhisho za changamoto za kijamii, na kuwa viongozi wenye maono.

Pia amesisitiza umuhimu wa kuzingatia maadili mema, uwajibikaji na uzalendo, akieleza kuwa mambo hayo ni msingi muhimu katika kujenga taifa imara na kuimarisha maendeleo ya Afrika kwa ujumla.

Hotuba yake imepokelewa kwa hisia chanya, ikichukuliwa kama ujumbe wa matumaini kwa kizazi cha vijana na wanawake wanaojitahidi kufikia mafanikio katika mazingira yenye changamoto mbalimbali.



SAME.

MAKAMU wa Rais na Waziri Mkuu mstaafu, John Samuel Malecela amesema kuwa, swala la Utalii kokote Duniani linaenda sambamba na swala la Amani na Utulivu na kuwaomba wananchi kuhakikisha wanalinda Amani ili kukuza Utalii nchi na kuendelea kujinufaisha kupitia sekta hiyo.

Malecela alitoa kauli hiyo jana wakati wa Uzinduzi wa tamasha la Same Utalii festival lililofanyika katika viwanja vya stendi wilayani Same mkoani Kilimanjaro ambapo alisema kuwa, utalii ni kite ambacho huchangia kuleta fedha za kigeni.

Alisema kuwa, baadhi ya nchi ulimwenguni serikali zinaendeshwa kwa fedha za Utalii na kuwataka kulichukulia swala hilo kwa umakini mkubwa.

Kiongozi huyo alidai kuwa, misingi ya Utalii ni ukarimu kwa wageni na kuwataka wananchi wa wilaya ya Same kuwa mfano katika ukarimu ili kukuza Utalii wa wilaya ya Same.

"Hata sehemu kukiwa na njiwa 10,000 wamejaa lakini jiwe likigonga tu wote wanakimbia kwa hiyo na sisi utalii wetu uanze na sisi wenyewe Watanzania kuwa na Amani ni jambo la msingi sana kwani Amani ndio italeta na kuwakaribisha watalii na ndio itatufanya tuendelee kukua kiuchumi" Alisema Malecela.

Na kuongeza "Swala la ukarimu kwa wageni ni kitu muhimu sana mahali pengine watu hawaendi kwa sababu hakuna moyo wa kuwapokea wageni lakini kwetu same tuwe na moyo wa kuwapokea wageni ili kukuza utalii wetu".

Alisema kuwa, kinachotuunga pamoja ni Amani na kuwasihi Watanzania kuendelea kuitunga na mambo mengine yatafuata.

"Ili Utalii wa same uweze kukua ni lazima uanze na sisi wenyewe wanasama kuwa na moyo dhabiti wa ukarimu ili wanapokuja na kurudi wakatoe sifa ni kweli wataenda kuona wanyama lakini mkiwakaribisha kwa moyo upande hawatarudi tena" Alisema Malecela.







Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo, amesema Tanzania inaendelea kujizatiti kusawazisha maendeleo ya kiuchumi, uendelevu wa mazingira, na usalama wa bahari.

Waziri Kombo amesema hayo alipozungumza katika Mkutano wa Tisa wa Bahari ya Hindi Aprili 10 2026, jijini Port Louis, Mauritius.

“Tanzania, kupitia juhudi za uhifadhi, ushirikishwaji wa jamii, na ushirikiano wa kikanda, inaendelea kulinda mifumo ya ikolojia ya bahari ya Hindi na kuimarisha usalama katika maji ya eneo lake, Ila mafanikio ya kudumu yatategemea ushirikiano imara zaidi kati ya nchi zinazopakana na bahari ya Hindi”, alisisitiza.

Balozi Kombo alihimiza nchi zinazopakana na bahari ya Hindi kuthibitisha wajibu wa pamoja na kushirikiana kuilinda bahari hiyo ili iendelee kuwa chanzo cha amani, ustawi, na fursa kwa vizazi vya sasa na vizazi vijavyo.

Alieleza kuwa Bahari ya Hindi ni nguzo muhimu ya ukuaji wa uchumi na ushirikiano wa kikanda kwa Tanzania, na ni lango muhimu linalounganisha nchi jirani zisizo na bandari na masoko ya dunia.

Aidha, alieleza kuwa kupitia uwekezaji wa kimkakati katika kuboresha na kuimarisha miundombinu ya bandari na nishati, Tanzania inaendelea kujiweka kama kitovu muhimu cha biashara, usafirishaji na huduma za baharini katika Afrika Mashariki na Kati na kwamba uchumi wa buluu unachangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya taifa, ukisaidia mamilioni ya watu na kukuza sekta za uvuvi, utalii, usafiri wa baharini na biashara za pwani.

Balozi Kombo alisema kaulimbiu ya mkutano huo ya “Uwajibikaji wa Pamoja kwa Usimamizi wa Bahari ya Hindi,” inaendana kikamilifu na hali halisi kwa sasa, na kwamba Bahari ya Hindi inakabiliwa na changamoto za mvutano wa kisiasa, vitisho vya usalama wa baharini vinavyoendelea kubadilika, pamoja na shinikizo la kimazingira.

“Changamoto hizi zinaonyesha umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya mataifa husika na kuwa uwajibikaji wa pamoja si hiari tena ni suala la lazima ili kuhakikisha kuwa bahari ya Hindi inakuwa salama, endelevu, na yenye manufaa kwa wote wanaoitegemea,” alisisitiza.














Top News