Mhandisi wa Miradi wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Mhandisi Edwin akizungumza na waandishi wa habari leo Januari 19, 2026 katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga

**
#Rais Samia Aendelea Kuimarisha Miundombinu


#Reli ya Kati kuboreshwa kwa Kiwango Kikubwa


#Mabwawa, Madaraja kujengwa


#Kutoka Makontena 400 Hadi 6,000


# Serikali yatoa Onyo Kali kwa Wahujumu Reli


Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog


Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeanza rasmi Awamu ya Pili ya Mradi wa Uboreshaji wa Reli ya Kati, mradi mkubwa wa kimkakati unaolenga kuhuisha reli ya zamani, kuongeza ufanisi wa usafirishaji wa mizigo na abiria, pamoja na kuimarisha uchumi wa taifa kwa kuifanya Bandari Kavu ya Isaka mkoani Shinyanga kuwa kitovu muhimu cha usafirishaji wa Kikanda.


Akizungumza na waandishi wa habari leo Januari 19, 2026 katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhandisi wa Miradi wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Mhandisi Edwin, mbele ya Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga David Lyamongi, amesema Serikali ya Tanzania imepokea dola za Marekani milioni 200, sawa na takribani shilingi bilioni 500, kwa ajili ya kugharamia shughuli za ukarabati na uboreshaji wa miundombinu ya reli ya zamani.


Mhandisi Edwin amesema reli ya kati ilijengwa tangu enzi za ukoloni na kwa muda mrefu imekuwa chakavu, hali iliyopunguza uwezo wake wa kuhudumia mizigo na abiria kwa ufanisi.


Amefafanua kuwa awamu ya kwanza ya mradi ilianza mwaka 2014 na kukamilika 2022, hata hivyo haikuweza kufikia malengo yote kutokana na upungufu wa rasilimali fedha, jambo lililosababisha Serikali kuja na awamu hii ya pili yenye wigo mpana zaidi.


Katika awamu hii ya pili, TRC itatekeleza shughuli mbalimbali ikiwemo utandikaji wa reli kwa takribani kilomita 392, katika kipande cha reli kuanzia Dar es Salaam hadi Isaka.


Kwa mkoa wa Shinyanga, kazi kubwa zitafanyika katika kipande cha Tabora hadi Isaka, ambapo reli zote chakavu zitaondolewa na kuwekwa reli mpya, nzito na zenye uwezo wa kupitisha treni ndefu na nzito zaidi.

Mhandisi wa Miradi wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Mhandisi Edwin.


“Tutafanya pia ukarabati mkubwa wa madaraja 171, ambayo yataongezewa uwezo wa kupitisha maji ili kuondoa changamoto za mafuriko. Aidha, kutakuwa na ujenzi na ukarabati wa mabwawa sita, pamoja na ujenzi wa mabwawa mawili makubwa yatakayojengwa na Serikali kupitia mapato ya ndani. Hivyo, jumla ya mabwawa yatakuwa nane, yatakayotumika kwa umwagiliaji, ufugaji wa samaki na matumizi mengine ya kiuchumi,” amesema Mhandisi Edwin.


Ameongeza kuwa katika utekelezaji wa mradi huo, TRC itashirikiana kwa karibu na Tume ya Taifa ya Umwagiliaji ili kuhakikisha uwekezaji huo unaleta manufaa mapana zaidi kwa wananchi.


Kwa mujibu wa TRC, matokeo ya mradi huu yanatarajiwa kuwa makubwa kiuchumi na kimkakati.


Kwa sasa, reli ya kati husafirisha wastani wa makontena 400 kwa mwaka kutoka Dar es Salaam hadi Isaka, lakini baada ya kukamilika kwa mradi, idadi hiyo inatarajiwa kuongezeka hadi makontena 6,000 kwa mwaka.

Aidha, muda wa upakiaji na upakuaji wa mizigo katika Bandari Kavu ya Isaka utapungua kutoka saa 10 hadi saa 4, kufuatia ukarabati wa miundombinu ya bandari hiyo.


Mhandisi Edwin pia amesema muda wa safari za treni za mizigo kutoka Dar es Salaam hadi Isaka utapungua kutoka wastani wa saa 50 hadi saa 30, hatua itakayopunguza gharama za usafirishaji na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya ndani na nje ya nchi.


Vilevile, mradi huu utaongeza njia za kupishania treni ili kuruhusu treni ndefu na nyingi zaidi kufanya safari kwa wakati mmoja.

Mhandisi wa Miradi wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Mhandisi Edwin.


Katika hatua nyingine, TRC itafungua milango kwa sekta binafsi, ambapo wawekezaji binafsi wataruhusiwa kuendesha treni zao katika miundombinu ya TRC. Hatua hiyo inalenga kuongeza matumizi ya reli, kuongeza idadi ya treni na kuboresha utoaji wa huduma kwa wateja.


Mradi huu umeanza rasmi Machi 2025 na unatarajiwa kukamilika mwaka 2029, huku huduma za reli zikiendelea kutolewa bila kusitishwa wakati uboreshaji ukiendelea.


“Tunayo SGR, lakini tumeamua pia kuboresha reli ya zamani ili zote zifanye kazi kwa ufanisi, kutokana na ongezeko kubwa la mahitaji ya usafirishaji wa mizigo,” amesisitiza.


Kwa upande wake, Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga, David Lyamongi, amesema mkopo wa shilingi bilioni 500 kutoka Benki ya Dunia ni fursa kubwa kwa mkoa wa Shinyanga na taifa kwa ujumla.

Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga, David Lyamongi


Amesema maboresho ya reli ya kati yataifanya Isaka kutumika rasmi kupokea makontena moja kwa moja kutoka Bandari ya Dar es Salaam, hatua itakayorahisisha nchi jirani kuchukua mizigo yao kupitia Tanzania.


Amewahimiza wananchi wa mkoa wa Shinyanga, hususan Halmashauri za wilaya za Manispaa ya Kahama na Msalala, kutumia fursa za ajira zitakazojitokeza wakati wa utekelezaji wa mradi huo, pamoja na kujihusisha na biashara ndogondogo na za kati zitakazohitajika kuhudumia mradi.


Ameongeza kuwa halmashauri zitanufaika kwa kupata vyanzo vipya vya mapato.


Lyamongi amesisitiza kuwa reli hiyo itaendelea kutoa huduma za usafirishaji wa mizigo na abiria, huku akionya kuwa Serikali imejipanga kikamilifu kuhakikisha usalama wa miundombinu na vifaa vyote.


“Yeyote atakayejihusisha na vitendo vya hujuma atachukuliwa hatua kali za kisheria, kwa sababu huu ni mradi mkubwa wa kitaifa wenye manufaa makubwa kwa taifa,” amesema.

Mhandisi Dkt. Veronica Mirambo


Katika kutoa mtazamo wa mazingira na jamii, Mratibu wa Masuala ya Mazingira na Jamii wa TRC, Mhandisi Dkt. Veronica Mirambo, amesema TRC itaendelea kutoa elimu kwa wananchi kupitia vijiji husika na vyombo vya habari kuhusu fursa za mradi, tahadhari za kiafya, na namna ya kujilinda dhidi ya hatari zinazoweza kujitokeza wakati wa utekelezaji wa mradi mkubwa.

Kamishna Msaidizi wa Polisi Batseba Kassanga


Naye Kamishna Msaidizi wa Polisi Batseba Kassanga, Afisa Polisi Jamii wa Kikosi cha Polisi Reli Tanzania, amesema TRC imejipanga kikamilifu katika suala la usalama wa wananchi, mazingira, miundombinu na mali za mkandarasi, ili kuhakikisha mradi unatekelezwa kwa amani na ufanisi.


Mradi huu unaonesha dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuendelea kuboresha miundombinu ya uchukuzi, kuimarisha reli ya kati na kuifanya Tanzania kuwa kitovu muhimu cha usafirishaji wa kikanda na kimataifa.

Mhandisi wa Miradi wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Mhandisi Edwin akizungumza na waandishi wa habari leo Januari 19, 2026 katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga

Mhandisi wa Miradi wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Mhandisi Edwin akizungumza na waandishi wa habari leo Januari 19, 2026 katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga

Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga, David Lyamongi akizungumza na waandishi wa habari

Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga, David Lyamongi akizungumza na waandishi wa habari

Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga, David Lyamongi akizungumza na waandishi wa habari
*Ni baada ya kukutana na kufanya naye mazungumzo nchini Norocco

*Amwambi Rais Samia yupo tayari kushirikiana na CAF kutekeleza mipango ya maendeleo ya soka



Na Mwandishi Wetu

WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Paul Christian Makonda amekutana na Rais wa Shirikisho la Kandanda Barani Afrika (CAF) Dkt. Patrice Motsepe Jijini Rabat, Morocco na kukabidhi barua kutoka kwa Rais Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Pamoja na kukabidhi barua hiyo Makonda aliyeongozana na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo na Msemaji Mkuu wa Serikali Bw. Gerson Msigwa amemhakikishia Dkt. Motsepe kuwa Rais Samia yupo tayari wakati wote kushirikiana na CAF katika utekelezaji wa mipango mbalimbali ya maendeleo ya kandanda ikiwemo mashindano mbalimbali.

Amesema Tanzania imepiga hatua kubwa katika maandalizi ya kuwa wenyeji wa AFCON 2027 sambamba na Kenya na Uganda na kwamba imedhamiria kuonesha tofauti kubwa na mashindano yaliyopita.

Aidha, Makonda amemuomba Dkt. Motsepe kuiangalia Tanzania kimkakati ili mipango inayowekwa na Serikali ipate mafanikio makubwa yanayotarajiwa.

Kwa upande wake Dkt. Motsepe amemshukuru Rais Samia kwa kumuandikia barua na salamu zake za upendo na ushirikiano kwa CAF na amemhakikishia kuwa CAF ipo tayari kufanya kazi bega kwa bega na Tanzania ili kufikia maendeleo makubwa katika kandanda.

Motsepe ameelezea kufurahishwa na jitihada kubwa zilizofanywa na Rais Samia na Serikali anayoiongoza katika maendeleo ya mpira ikiwemo ujenzi wa miundombinu, kufanya mashindano ya CHAN 2024 kwa mafanikio makubwa na maandalizi mazuri yanayoendelea kuelekea AFCON 2027.

Amesema CAF itatuma timu ya wataalamu kwenda Tanzania kushirikiana na Serikali na wadau mbalimbali katika kukamilisha maandalizi makubwa ya AFCON 2027 ambayo yanatarajiwa kushirikisha nchi 28 badala ya 24.

Motsepe ameahidi kuja Tanzania hivi karibuni kujionea maandalizi mbalimbali ya AFCON 2027 na kukutana na viongozi kwa mazungumzo.







Na. OWM-KAM – Dodoma

Bodi ya Wadhamini ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) imetakiwa kuweka mikakati ya kuanza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ili mfuko uchangie katika kutoa huduma bora zaidi ikiwemo kuongeza uzalishaji ajira kwa sekta binafsi.
Akizungumza katika kikao hicho, Januari 17, 2026 Jijini Dodoma Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu alisema Serikali kupitia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inalenga kuanzisha na kuimarisha mfumo jumuishi wa hifadhi ya jamii utakaojumuisha sekta isiyo rasmi. 

“Hatua hiyo itachochea uwekezaji katika miradi ya maendeleo, kuongeza wigo wa ulinzi wa kijamii na kuimarisha uzalishaji wa ajira kwa Watanzania wengi” amesema.
Mhe. Sangu alisema Serikali kuanzia mwezi Julai mwaka huu itaanza utekelezaji wa Dira 2050 ambapo kwa sekta ya hifadhi ya jamii dhima mojawapo ni kuhakikisha ukuaji wa Uchumi Jumuishi na uzalishaji wa ajira unapewa kipaumbele kupitia sekta binafsi.

Katika hatua nyingine. amesema katika mpango wa kwanza wa maendeleo wa miaka mitano utakaochangiwa sekta binasfsi inatakiwa kuchangia asilimia 70 ambapo Mfuko wa WCF unatakiwa kuongeza wigo wa kuandika wanachama toka sekta binafsi ili kiwango cha uchanguaji kikue zaidi.

“ Tuitazame sekta binafsi kama kiungo cha kukuza Uchumi ambapo mfuko wa WCF unapaswa kubuni na kuwekeza kwenye miradi ya kimakakati ambayo itaongeza kasi ya uzalishaji ajira ili mfuko upate wachangiaji wengi zaidi na kuufanya uendelee kuwa himilivu” alisisitiza Waziri Sangu.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) Renata Rugarabamu alimweleza Waziri kuwa mfuko huo ni himilivu na kwamba unaendelea kutoa huduma zake kwa wafanyakazi kwa weledi na ubora.

Rugarabamu aliongeza kusema Mfuko wa WCF utaendelea kuhakikisha wafanyakazi waliopata majanga inawapa fidia ili waweze kurudi katika jamii kuendelea kutoa mchango wao kwenye ukuaji wa uchumi ambapo alibainisha kuwa mfuko umeongezeka toka shilingi Bilioni 26 mwaka 2024 hadi shilingi Bilioni 51 mwaka 2025 hatua inayoufanya uwe  himilivu.

Waziri Sangu alikutana na Bodi hiyo ikiwa ni mara ya kwanza tangu alipoteuliwa kuwa Waziri mwenye dhamana ya sekta ya kinga ya jamii ambapo Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) ni moja wapo. Taasisi zingine zinazotekeleza kinga ya jamii ni Mfuko wa Pensheni kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF).











Wanakwaya wa Mt. Joseph, Parokia ya Bikira Maria wa Mlima Karmel Bunju, jimbo la Bagamoyo wameaswa kutumia vema mitandao ya kijamii kutangaza kwaya yao na ujasiriamali ili kujiongezea kipato.

Wito huo umetolewa Januari 18,2026 Parokiani hapo na Msemaji wa kwaya hiyo Bi. Rose Ngunangwa wakati wa mafunzo kwa wanakwaya hao ambapo amesisitiza pia umuhimu wa kuwa na nidhamu na kuheshimu utu mitandaoni.


“Kama vijana wa kikatoliki na wanakwaya ninawaasa kuheshimu utu wa watu mitandaoni na kutochangia kutweza, kudhalilisha au kutusi mtu. Tumieni mitandao kunadi kazi zenu ili kuongeza kipato. Naomba msiwe watumwa wa historia hata kama hukubahatika kufanya vema kwenye masomo tumia karama ulizonazo kutengeneza kipato,” amesisitiza.


Katika miaka ya hivi karibuni, kwaya ya Mt. Joseph Bunju imejipatia umaarufu mkubwa katika uimbaji huku baadhi wakiita Tanzania 2 kutokana na uimbaji wenye sauti zilizopangiliwa.


Kwa sasa kwaya hiyo inatamba na nyimbo zake mpya kama Ishara ya Msalaba na Nia Yangu, nyimbo ambazo zinafanya vema kwenye majukwaa mbalimbali ya kidijitali.


Kwaya hiyo imeweza kushiriki matamasha makubwa ya kitaifa kama Mkatoliki Concert, Tamasha la Yesu ni Mwema na lile la Jubilei ya Miaka 25 ya Uaskofu wa Mhashamu Augustine Shao wa Zanzibar ambapo ilijizolea mashabiki lukuki visiwani humo.
ISHARA YA MSALABA || KWAYA YA MT. JOSEPH - BUNJU || OFFICIAL VIDEO.


NIA YANGU (Official Video) | Mt. Joseph Bunju


Wakati anamsifia mpenzi wake Msanii Mbosso aliimba “ Kamusi namaliza kurasa kukusifia” ,na akahitimisha kwa kusema anaishiwa pawa kwa kuwa penzi la huyo ampendaye ni mizani nzito.

Mbosso angepata fursa ya kupanda mlima Lolmalasin uliopo Ngorongoro kamwe asingeishiwa pawa, badala yake angeongeza maneno katika kamusi kuusifia mlima huu unaopatikana katika kivutio namba moja cha utalii barani Afrika.

Angeusifia mlima huu kwa kuwa ni mlima mrefu zaidi ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro na mlima wa tatu kwa urefu Tanzania, ukiwa na kimo cha mita 3,700 kutoka juu ya usawa wa bahari.

Angepanda mlima huu asingeweza kuishiwa pawa kutokana na mandhari yaliyopambwa na maua, miti, ndege, wanyama huku akishuhudia Kreta ya Olmoti kwa mbali ikitiririsha maji yake kwenda Kreta ya Ngorongoro kupitia mto Munge.

Mlima huu si mzuri tu kupanda laah hasha, unakusaidia kupiga jaramba na kunyoosha misuli hasa kwa wanaojiandaa kukwea Milima mirefu kama Meru na Kilimanjaro.

Ukipanda mlima huu si tu unajenga afya na kupanua mawanda ya upeo wa macho na akili yako, bali utahisi upo peponi na kusahau changamoto zote ikiwemo Stress za ada za januari, vikoba, kazi na hata mapenzi.

Na kama Mbosso alisema kwamba yeye ni Mjusi anaparamia ukuta wa plasta basi hata watalii kutoka maeneo mbalimbali wanaweza kuupanda mlima huu bila kuuparamia na wala hawataishiwa Pawa kamwe.

Karibuni wageni kupanda mlima Lolmalsin, Ngorongoro inawahakikishia kutoishiwa pawa na badala yake pawa zitaongezeka maradufu.

Tuishie hapa kwa methali isemayo " Kinywa ni Jumba la Maneno " kesho kutoka Ngorongoro tutakuletea maneno ya kivutio kingine cha utalii kwa kuwa "Jungu kuu halikosi ukoko"

Maajabu ya Ngorongoro yanakuita,

Uzoefu usiosahaulika,

Tumerithishwa, Tuwarithishe.


Meneja mauzo wa Vodacom Tanzania Plc wilaya ya Mbarali mkoani Mbeya Happyness Lyimo ( wa pili kulia) pamoka na afisa wa kampuni hiyo Wema Mpwanga ( kulia), wakikabidhi Kapu la Voda kwa mzazi Martin Daud Sanga (Kushoti) na Mwanafunzi Jastin Daud Sanga (wa pili Kushoto). 

Tukio hili ni muendelezo wa kampeni ya "Tupo nawe Tena na Tena" ambayo inalenga kugawa makapu yenye vifaa vya shule kwa wateja wao, ambapo msimu huu unalenga wazazi na wanafunzi wanaorudi mashuleni . Kampeni hiyo imeendelea kugawa makapu hayo sehemu mbalimbali nchini, na ikilenga kuwaunga mkono wazazi wanaopeleka watoto wao shuleni kwa mwaka mpya wa masomo kwa kuwapa baadhi ya vifaa vya shule vitakavyo wawezesha watoto kuendelea na masomo yao. Hafla hii imefanyika jijini Mbeya, Mwishoni mwa wiki.




-Asema lengo ni kujenga Taifa lenye hofu ya Mungu, upendo, haki na uwajibikaji

 

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Januari 18, 2026 ameshiriki Ibada ya Jumapili katika Kanisa Kuu Anglikana la Roho Mtakatifu Dodoma na amesisitiza kwamba Serikali itaendelea kushirikiana na viongozi wa dini kujenga Taifa lenye hofu ya Mungu, upendo, haki na uwajibikaji.

“Sote tunatambua kwamba Taasisi za dini zina nafasi ya kipekee ya kuhubiri na kufundisha maadili ya upendo, uvumilivu na kuheshimiana, ambazo ni nguzo kuu za amani ya Taifa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anatambua na kuthamini sana mchango mkubwa wa taasisi za dini ikiwemo Kanisa la Anglikana, katika kudumisha amani, maadili mema na mshikamano wa Kitaifa.

 Pia, Waziri Mkuu amesema kuwa ibada za Jumapili ni sehemu muhimu ya maisha ya Mkristo na ni muda wa kujitathmini, kuimarisha mahusiano yao na Mwenyezi Mungu, na kujifunza namna bora ya kuishi kwa mujibu wa mapenzi ya Mwenyezi Mungu katika familia, jamii na Taifa kwa ujumla.

 Amesema Watanzania wanakumbushwa kuishi kwa misingi ya upendo, unyenyekevu, haki na uwajibikaji kwani Biblia inasisitiza wazi kuwa “Umejulishwa, ee mwanadamu, yaliyo mema; na Bwana anataka nini kwako, ila kutenda haki, kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu mbele za Mungu wako” (Mika 6:8) na maadili hayo si ya kidini pekee, bali ni msingi muhimu wa ustawi wa jamii na maendeleo ya Taifa.

 Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amesema Tanzania imeendelea kuwa kielelezo cha amani, umoja na mshikamano katika ukanda wetu na barani Afrika. “Amani hii si jambo la bahati, bali ni matokeo ya jitihada za pamoja za Serikali, taasisi za dini, familia na wananchi kwa ujumla.”

 Waziri Mkuu amesisitiza kuwa imani wanayojifunza na kuimarisha katika ibada inapaswa kutafsiriwa katika matendo ya uadilifu, uwajibikaji, bidii katika kazi, kuheshimu sheria na kushiriki kikamilifu katika kujenga Taifa lenye haki, amani na maendeleo endelevu. “Imani ya kweli inapaswa kuonekana kwa matendo.”

Kadhalika, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu ametumia fursa hiyo kutoa wito kwa waumini wote na Watanzania kwa ujumla kuendelea kuwa mabalozi wa amani katika familia zao, maeneo ya kazi na katika jamii kwa ujumla kupinga vitendo vyovyote vya chuki, migawanyiko na vurugu.

 Awali, Askofu wa Kanisa Anglikana Tanzania, Dayosisi ya Central Tanganyika, Dk. Dickson Chilongani ameipongeza Serikali kwa kuendelea kushirikiana na taasisi za kidini likiwemo Kanisa Anglikana na kwamba wapo pamoja na nayo katika kuhakikisha nchi inaendelea kuwa na amani. “Tunataka nchi iwe na amani ili shughuli ziendelee na hatutachezea amani.








📍Wiki ya Huduma za fedha Kitaifa kuanza viwanja vya Usagara Tanga



Na MASHAKA MHANDO, Tanga

Wizara ya Fedha imetangaza rasmi kuanza kwa maadhimisho ya Wiki ya Huduma za Fedha Kitaifa mkoani Tanga, yenye lengo la kuwajengea wananchi uwezo wa kusimamia uchumi wao na kuongeza uelewa wa masuala ya fedha nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari mkoani hapa leo, Kaimu Kamishina wa Idara ya Uendelezaji wa sekta za fedha wa Wizara ya Fedha, Dionesia Mjema msemaji ameeleza kuwa maadhimisho hayo yatafanyika katika Viwanja vya Usagara kuanzia Januari 19 hadi Januari 26, 2026.

Tukio hilo linatarajiwa kuzinduliwa rasmi na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb).

Alisema malengo ya Serikali kwa maadhimisho haya ni sehemu ya utekelezaji wa Mpango Mkuu wa Maendeleo ya Sekta ya Fedha (2020/21 – 2029/30).

Alisema serikali ya Awamu ya Sita, chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, imedhamiria kuhakikisha ifikapo mwaka 2025, asilimia 80 ya Watanzania wanakuwa na uelewa wa masuala ya fedha.

"Utafiti wa FinScope wa mwaka 2023 ulionyesha kuwa ni asilimia 53.5 tu ya nguvu kazi ndiyo inayotumia huduma rasmi za fedha. Tunataka kuwafikia wale ambao bado hawajafaidika na huduma hizi ili waboreshe maisha yao na kukuza Pato la Taifa," alisema Mjema.




Nini Kitatokea Usagara?

Chini ya kauli mbiu isemayo "ELIMU YA FEDHA, MSINGI WA MAENDELEO YA KIUCHUMI," wananchi watakaofika viwanjani hapo watapata elimu ya bure kuhusu Usimamizi wa fedha binafsi na uwekaji akiba.

Pia watajifunza utaratibu wa kukopa na kulipa madeni,Elimu ya kodi, bima, na bima ya amana,Uwekezaji katika hatifungani na masoko ya mitaji na Ulinzi wa mtumiaji wa huduma za fedha.

Alisema washiriki na Walengwa wa tukio hilo lilobeba mwavuli mpana wa wadau, likijumuisha Wizara mbalimbali kutoka Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Benki, Taasisi za bima, na asasi za kiraia.

Walengwa wakuu ni pamoja na wajasiriamali wadogo na wa kati (SMEs), wanawake, vijana, watu wenye mahitaji maalumu, wanafunzi, na watumishi wa umma.

Alisema mbinu mbalimbali kama semina, maonesho ya bidhaa, na majukwaa ya kidigitali zitatumika kufikisha ujumbe kwa wananchi watakaofika kwenye viwanja vya Usagara Jijini Tanga.

Alisema Wizara ya Fedha inatoa wito kwa wakazi wa Tanga na mikoa ya jirani kujitokeza kwa wingi kupata maarifa hayo ambayo yatatolewa na wataalamu wabobezi bila malipo yoyote.

"Hii ni fursa ya kipekee kwa mjasiriamali na mwananchi mmoja mmoja kuunganishwa na fursa za sekta ya fedha ili kukuza biashara na kuimarisha uchumi wa kaya," alisema.







Top News