Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limepokea msaada wa gari maalum lenye maabara inayotembea kutoka Ubalozi wa Sweden, hatua inayolenga kuimarisha usimamizi na utekelezaji wa Sheria ya Mazingira nchini.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Februari 19, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa makabidhiano hayo, Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Immaculate Semesi, amesema kuwa kabla ya kupatikana kwa msaada huo, baraza lilikuwa likitumia gharama kubwa na muda mrefu kuchukua sampuli na kuzipeleka katika maabara nyingine kwa ajili ya upimaji.
“Maabara hii inayotembea, yenye thamani ya shilingi milioni 715, italeta ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yetu kwa njia tatu kuu: kupunguza gharama, kuokoa muda, na kuongeza ubora wa maamuzi ya kitaalamu,” amesema Dkt. Semesi.
Amefafanua kuwa awali ililazimu sampuli kusafirishwa kwenda maabara zilizothibitishwa, jambo lililosababisha ucheleweshaji wa maamuzi. Kupitia maabara tembezi, upimaji sasa utaweza kufanyika papo hapo eneo la tukio.
Aidha, Dkt. Semesi amesema NEMC ina kanda 13 nchini, na matarajio ni kupata angalau magari 12 zaidi ya maabara tembezi ili kuimarisha huduma katika mikoa yote na kuhakikisha ukaguzi unafanyika kwa haraka na kwa ufanisi zaidi.
Kwa upande wake, Mratibu wa Mradi huo, Paul Kalokola, amesema gari hilo lina vifaa vya kisasa, ikiwemo droni zitakazosaidia kufikia maeneo magumu au yaliyofichika.
“Teknolojia hii itawezesha upimaji wa kisayansi kufanyika popote nchini na kusaidia maamuzi yanayotegemea ushahidi wa kitaalamu,” amesema Kalokola.
Naye Meneja wa Programu za Mazingira na Hali ya Hewa kutoka Ubalozi wa Sweden, Stephen Mwakifwamba, amesema mradi huo ulikuwa na thamani ya dola milioni tatu za Marekani. Amesema mradi huo haukujumuisha tu ununuzi wa maabara tembezi, bali pia uboreshaji wa sheria na kanuni za mazingira pamoja na kuzitafsiri kwa Kiswahili ili ziweze kueleweka kwa wananchi.
Ameishauri NEMC kuhakikisha vifaa hivyo vinatunzwa na kufanyiwa matengenezo ya mara kwa mara ili vidumu na kutoa huduma kwa muda mrefu.
Serikali ya Sweden imeahidi kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kuimarisha uhifadhi wa mazingira kwa maendeleo endelevu na ustawi wa wananchi.
Maabara hiyo imenunuliwa kupitia mradi wa miaka mitatu uliofadhiliwa na Serikali ya Sweden kupitia Shirika la Maendeleo la Sweden, uliolenga kujenga uwezo wa taasisi za serikali na binafsi katika usimamizi wa mazingira.













.jpeg)


.jpeg)




.jpeg)

.jpeg)







.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)

