Serikali imewataka vijana wanaopata fursa za ajira nje ya nchi kuwa mabalozi wa Taifa kwa kuzingatia nidhamu, uadilifu na tamaduni katika nchi wanazokwenda, ili kulinda heshima ya Tanzania.

Wito huo umetolewa na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Rahma Kisuo, leo Februari 07, 2026 katika ukumbi wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya kuwaaga rasmi vijana 200 wanaoenda kufanya kazi nje ya nchi.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Kisuo amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuimarisha mifumo ya kisheria na kitaasisi ya kusimamia ajira nje ya nchi, kwa lengo la kuhakikisha Watanzania wanapata ajira zenye staha.

Ameeleza kuwa, Serikali imeendelea kuratibu na kusimamia shughuli za Mawakala Binafsi wa Ajira waliosajiliwa, ambao wanauganisha Watanzania na fursa za ajira nje ya nchi kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizopo.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Huduma za Ajira, Jane Sorogo, amewashukuru Mawakala Binafsi wa Ajira kwa namna wanavyoshirikiana na Serikali katika kuwaandaa vijana wanaopata fursa za ajira nje ya nchi.

Naye, Makamu Mwenyekiti wa Mawakala wa Ajira nchini, Rashid Milao, ametoa wito kwa vijana waliopata fursa hizo za ajira kuzingatia maelekezo wanaliyopewa na Serikali ili kuiwakilisha vyema Tanzania kimataifa.


Mwenyekiti wa halmashauri ya Mji Handeni, Amiri Mwaliko,akizungumza katika mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju,akizungumza katika mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.

Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Reuben Kwagilwa,akiteta jambo na Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese,wakati wa  mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.

Sehemu ya Madiwani wakifuatilia mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.

Na Augusta Njoji

MWENYEKITI wa Halmashauri ya Mji Handeni, Mhe. Amiri Mwaliko, amempongeza Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan, kwa kutoa kibali cha ajira kilichowezesha kupatikana kwa watumishi 82 wa kada mbalimbali na hivyo kupunguza uhaba wa watumishi katika halmashauri hiyo.

Akifungua mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata wa Halmashauri hiyo uliofanyika Februari 7, 2026 mjini hapa, Mhe. Mwaliko amesema serikali imeendelea kuchukua hatua za kutatua changamoto ya upungufu wa watumishi.

“Tunaishukuru serikali kwa kuendelea kutatua changamoto ya watumishi. Tunafurahia hatua hii kwa kuwa lengo la serikali ni kuondoa uhaba wa watumishi na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi,” amesema.

Aidha, amempongeza Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, kwa kuhakikisha wilaya hiyo inaendelea kudumisha amani na utulivu.

Mhe. Mwaliko amewataka viongozi na watumishi kushirikiana katika kujenga halmashauri yenye mshikamano na kutatua changamoto zinazojitokeza.

Ameongeza kuwa ni muhimu kusimama pamoja na watumishi na kushughulikia changamoto kwa njia ya mazungumzo ili kujenga timu imara ya utendaji kwa maendeleo ya halmashauri.

Kadhalika, amesisitiza kuendelea kuchukuliwa hatua za kudhibiti utoro wa wanafunzi kwa kushirikiana na madiwani wa maeneo husika.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju, amesema katika mwaka wa fedha 2025/26 serikali imeajiri watumishi 82 wakiwemo walimu wa shule za msingi na sekondari pamoja na wauguzi.

Amesema changamoto ya upungufu wa watumishi inaendelea kupatiwa ufumbuzi kadri serikali inavyoendelea kutoa ajira, huku halmashauri ikiendelea kutenga bajeti kupitia mapato ya ndani kwa ajili ya kuchangia maendeleo ya kata, ikiwemo ununuzi wa madawati.


Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Reuben Kwagilwa,akizungumza katika mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.

Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese,akizungumza katika mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju,akizungumza katika mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.

Mwenyekiti wa halmashauri ya Mji Handeni, Amiri Mwaliko,akizungumza katika mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.

Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Reuben Kwagilwa,akiteta jambo na Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese,wakati wa  mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.

Sehemu ya washiriki wakifatilia hotuba ya Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Reuben Kwagilwa (hayupo pichani) wakati wa mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.

Na Augusta Njoji

Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Reuben Kwagilwa, ameelekeza taasisi za serikali zinazohudumia wananchi wilayani Handeni kuwasilisha taarifa za utekelezaji wa majukumu yao katika Baraza la Madiwani ili kuongeza uwazi na kuwafanya wananchi kufahamu kazi zinazofanywa na serikali.

Akizungumza katika mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika Februari 7, 2026, Mhe. Kwagilwa amesema ni muhimu kwa wakuu wa taasisi za serikali kuhudhuria vikao vya Baraza la Madiwani na kuwasilisha taarifa zao.

Amezitaja baadhi ya taasisi hizo kuwa ni pamoja na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA), Mamlaka ya Maji pamoja na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), akisisitiza kuwa taasisi hizo zinawajibika moja kwa moja kwa wananchi.

Pamoja na hayo, amempongeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju, pamoja na wataalamu wa halmashauri hiyo kwa mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) iliyopita na kuendelea kutekeleza ilani ya sasa.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Mhe. Amiri Mwaliko, amempongeza Naibu Waziri Kwagilwa kwa kuaminiwa na Rais Samia Suluhu Hassan kushika nafasi hiyo, akisema anaamini atatekeleza vyema majukumu yake katika kuisaidia TAMISEMI.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe.Salum Nyamwese ameahidi kuwapa ushirikiano Madiwani katika utekelezaji wa majukumu yao.

\

Kassim Nyaki, Ndutu Ngorongoro.

Waswahili husema aungurumapo Simba mcheza nani?

Tarehe 7 Februari, 2026 Simba ameunguruma  ndani ya hifadhi ya Ngorongoro eneo la Ndutu kwa uzinduzi wa Chapa mpya ya Destination Ngorongoro.

Kamishna wa Uhifadhi mamlaka ya Hifadhi ya eneo la Ngorongoro (NCAA) Abdul-Razaq Badru ameongoza Menejimenti ya mamlaka hiyo na wadau mbalimbali wa sekta ya utalii kuzindua  Utambulisho Mpya wa Chapa ya “Destination Ngorongoro” inayoashiria mwanzo mpya wa maajabu ya Ngorongoro ambayo kwa miongo mingi imekuwa ikivutia dunia kwa uzuri wake wa kipekee.

Akizindua utambulisho huo katika eneo la Ndutu  Ngorongoro, Kamishna Badru ameeleza kuwa kabla Ngorongoro haijawa kivutio cha utalii kinachotambuliwa duniani, ilikuwa ni sauti yenye mwito wa uhai unaounganisha Wanyamapori, utamaduni, ardhi, historia ya mwanadamu, malikale, mazingira na maumbo mbalimbali yanayoiakisi dunia ilipojikunja na kuunda Kasoko ya Ngorongoro.

“Katika dunia ambayo ushindani wa vivutio vya utalii ni mkubwa unaozidi kuwa na Faru, tembo  na visukuku pekee, Ngorongoro imeamua kujipambanua zaidi kwa mwito wenye dhamana na wajibu ndio maana tunawatambulisha rasmi muonekano mpya wa chapa ya Destination Ngorongoro kwa kufanya maboresho ya namna Ngorongoro inavyojitambulisha kwa dunia na kwa wageni kwa umahiri na muonekano ulioboreshwa” amefafamua kamishna Badru.

Moja ya maajabu ya kipekee ya asili duniani ni tukio la kuzaliana kwa nyumbu  eneo la Ndutu ambapo kila baada ya saa moja takribani ndama 80,000 huzaliwa. 

Katika Bonde la Olduvai na Laetoli, historia na nyayo za kwanza za binadamu zilipatikana zikitukumbusha kuwa Ngorongoro si hadithi ya wanyamapori pekee, bali ni Chimbuko la binadamu, hii ni ishara kuwa Ngorongoro ni maajabu yanayopaswa kusimuliwa hatua kwa hatua na  Ngorongoro sio tu unatazamwa bali inabaki na kuishi mioyoni mwa watu.

Kamishna Badru amebainisha kuwa maboresho ya chapa ya Ngorongoro hayapo kwenye muonekano pekee bali pia yanasimuliwa kwa hadithi za Ngorongoro ili wageni wa mataifa mbalimbali wanapogika  Ngorongoro kuielewa kwa undani zaidi. 

Simulizi za maajabu ya Ngorongoro zinaenda sambamba na  kuimarisha nyenzo kidijitali kwa uwazi zaidi na  upeo wa kimataifa ambapo Ngorongoro inazungumza kupitia hadithi moja iliyounganisha  mazingira hai historia ya binadamu, utamaduni, na asili na kuzungumza kwa sauti moja, mtindo mmoja, na utambulisho mmoja.

Badru anabainisha kuwa mwaka 2026 utakuwa Mwaka wa Maajabu,

chini ya kauli mbiu isemayo “Wonders Are Calling” ambayo itatekelezwa kwa awamu ikifichua maajabu ya Ngorongoro kwa kila msimu utaangazia ajabu tofauti.

Jee Maajabu hayo yatayofichuliwa kwa awamu yatakuwa ni yapii? Fuatana nasi katika taarifa zetu zijazo.

Enzi mpya ya Maajabu imeanza.

Mwito umetolewa.

Destination Ngorongoro, Experience the Wonders.





 

NA DIANA DEUS_BUKOBA.

Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalumu ya Kiuchumi Tanzania (TIZESA) imewaahidi wawekezaji wazawa kuanzisha madawati ya uwekezaji katika kila halmashauri, yatakayounganisha taasisi zote zinazohusika na usajili wa masuala ya uwekezaji ili huduma zote zipatikane katika dawati moja na kurahisisha hatua za kuanza uwekezaji.

Taasisi ya TIZESA inaendelea na kampeni maalum ya kuhamasisha uwekezaji kwa lengo la kusogeza huduma za uwekezaji hadi ngazi ya mikoa na halmashauri, na kuhakikisha kila Mtanzania anapata fursa ya kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa uchumi wa taifa.

Akizungumza katika kongamano la wadau wa uwekezaji wa ndani mkoani Kagera, Mwenyekiti wa Bodi ya TIZESA, Balozi Azizi Mlima, amesema taasisi hiyo imelenga kutoa elimu ya uwekezaji kwa wananchi ili kuwawezesha kupata unafuu wa mitaji, pamoja na kusimamia utekelezaji wa sheria na taratibu za uwekezaji, ikiwemo kuwapunguzia adha wawekezaji kwa kuweka dawati moja la kupata huduma zote.

Ameeleza kuwa licha ya changamoto ya uelewa mdogo wa uwekezaji kwa baadhi ya Watanzania, elimu na mipango ya TIZESA imeanza kuzaa matunda kwa kuwahamasisha wananchi kuwekeza zaidi ndani ya nchi, kupunguza utegemezi wa bidhaa kutoka nje na kukuza uzalishaji wa ndani.

Amesema TIZESA inaangazia fursa mbalimbali katika Kanda ya Ziwa, ikiwemo mkoa wa Kagera ambako kuna fursa nyingi za uwekezaji zikiwemo kilimo cha mazao ya biashara kama maparachichi, ufugaji wa kisasa, ufugaji wa samaki na uongezaji thamani wa mazao ya kilimo.

Aidha, wananchi wamekumbushwa umuhimu wa kumiliki hati za nyumba na viwanja kama nyenzo muhimu ya kupata mikopo kutoka taasisi za kifedha na kuanzisha au kupanua miradi ya uwekezaji.

Wawekezaji walioshiriki kongamano hilo wamepongeza hatua za TIZESA kuona umuhimu wa kufikisha elimu na kuweka mpango wa kufungua madawati ya uwekezaji katika ngazi ya halmashauri, wakieleza kuwa ni hatua muhimu ya kutambua changamoto zao katika uwekezaji na kurahisisha hatua za kujisajili katika uwekezaji.








📍 Ammwagia sifa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kuboresha miundombinu


Na Mwandishi Wetu, Mbeya

MABORESHO yanayofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita katika sekta ya elimu yameendelea kuzaa matunda baada ya ufaulu wa wanafunzi kuongezeka kwa kasi nchini. 

Akizungumza na wadau wa elimu Jijini hapa, Mkuu wa wilaya ya Mbeya Mhe Solomon Itunda alisema maboresho katika sekta ya elimu yamesaidia kwa kiasi kikubwa kuongezeka kwa ufaulu nchini.

Itunda alisema hatua hiyo imetokana na  uamuzi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kutoa mabilioni ya fedha kwa ajili ya ujenzi wa madarasa, maabara, na uboreshaji wa mazingira ya kufundishia, jambo ambalo limerejesha hamasa ya kusoma kwa wanafunzi na walimu.

Alisema katika kuyaenzi maboresho hayo na kuhakikisha tija inaonekana darasani, Mkuu huyo wa wilaya amewaeleza wadau wa elimu Jijini Mbeya kwamba ni vema kuweka mkakati wa kudumu wa ustawi wa wanafunzi ikiwemo kuhakikisha kila shule watoto wanapata chakula cha mchana kuboresha afya ya Mwanafunzi.

Hivyo, Mkuu huyo wa wilaya akawaagiza  Watendaji wa Kata na Maafisa Tarafa kuhakikisha kila mzazi na mlinzi anatimiza wajibu wake wa kuchangia chakula shuleni. 

"Serikali imeshajenga madarasa na kuboresha mazingira; wajibu wa mzazi ni kuhakikisha mtoto ana nishati ya kusoma. Watendaji msimame imara, wazazi watakaokaidi agizo hili wachukuliwe hatua mara moja," alisisitiza Mhe. Itunda.

Mbali na lishe, kikao hicho kimepitisha mikakati mipya ya kupandisha kiwango cha ufaulu ndani ya Jiji la Mbeya kwa kuimarisha usimamizi wa taaluma na ujenzi wa ushirikiano wa "pande tatu" kati ya walimu, wazazi, na viongozi wa mitaa. 

Pia Mkuu huyo wa wilaya amewapongeza walimu wa shule za za Jiji la Mbeya kwa uzalendo wao na kazi kubwa ya kulea taifa, akiwataka wasirudi nyuma katika jukumu hilo takatifu.

Akihitimisha, Mkuu wa Wilaya amemshukuru na kumpongeza kwa dhati Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha nyingi kwa ajili ya miundombinu na uimarishaji wa maslahi ya walimu ambao wamepelekea  Jiji la Mbeya kuimarika kielimu, na kuahidi kuwa wilaya yake itahakikisha uwekezaji huo unaleta matokeo ya daraja la kwanza kwa kila mwanafunzi.

DC Itunda ahimiza chakula mashuleni Mbeya





-Rais Samia amhakikishia Rais Museven utayari wa Tanzania katika kushirikiana na Uganda kuleta maendeleo

*Azungumzia ujenzi wa reli ya SGR,atoa ombi kwa Museven,wazungumzia hali ya usalama iliyopo sasa




Na Said Mwishehe,Michuzi Blog.

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Samia Suluhu Hassan ameeleza masuala mbalimbali ambayo wamezungumza na Rais wa Uganda Yoweri Museven huku akimhakikishia utayari wa Tanzania katika kutoa kila aina ya ushirikiano kwa lengo la kufanikisha maendeleo ya nchi hizo mbili.

Aidha amemhakikishia ambavyo Tanzania imejipanga vema katika ujenzi wa miundombinu ya usafirishaji ikiwemo ujenzi wa reli ya kisasa kwa lengo la kurahisha usafiri kati ya nchi hiyo na nchi nyingine za Afrika Mashariki ikiwemo nchi ya Uganda.

Akizungumza leo Februari 7,2026 ,Ikulu jijini Dar es Salaam na waandishi wa habari baada ya kufanyika mazungumzo baina ya marais hao,Rais Dk.Samia amesema katika mazungumzo yao wamejadiliana masuala mbalimbali.

“Tumezungumzia kuhusu bomba la kusafirisha mafuta kutoka Tanzania kupeleka Uganda lakini kuna bomba la mafuta safi sasa ambayo yatakuwa yamesafishwa Uganda yanakwenda kwenye nchi yanayouzwa.

“Tutatumia korido hiyo hiyo kusafirisha mafuta hayo safi kutoka Uganda hadi Tanga na kisha kusafirishwa huko yanakopelekwa.Pili kama mnavyojua nchi zetu ambazo hazina bahari wanategemea sana bandari za Tanzania ikiwemo bandari ya Dar es Salaam na bandari ya Tanga.

“…hata bandari ya Mtwara lakini kwa Uganda ni bandari ya Dar es Salaam na Tanga hivyo tumezungumza jinsi watakavyopata nafasi ya kuzitumia bandari hizi na kusafirisha mizigo.

“Kubwa zaidi tumewapa taarifa Tanzania ndani ya Ilani ya Chama Cha Mapinduzi katika kipindi hiki mpaka 2030 tuna nia ya kujenga reli itakayounganisha Mkoa wa Tanga hadi Musoma na kule watasafirisha kwa ziwa kwenda Uganda.”

Rais Dk.Samia amesema jambo ambalo limewapa faraja sana Uganda wakati wa mazungumzo yao kwani usafiri utakuwa umerahisishwa.

Pia amesema wamezungumza kuhusu reli ya SGR ambayo itajengwa mpaka Isaka na kisha hadi Lusahunga hivyo wamewaomba Uganda waunge hapo kuelekea Murongo na kwenda mbele ndani ya Uganda.

“Hilo ni ombi letu tumewapa ili kuunganisha sasa ile reli iliyokusudiwa kwenda Burundi na DRC sasa tunapeleka mpaka Lusahunga ili Waganda waunge pale kwenda katika nchi yao kwa lengo la kurahisisha upatikanaji wa bidhaa.

“Pia kama mnavyoelewa meli yetu ya MV Mwanza imeanza kufanya kazi ndani ya ziwa na bila shaka itakwenda kuhudumia na Uganda,”amesema Rais Dk.Samia alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari akielezea waliyozungumza na Rais Museven .

Pia amesema wamezungumza kuhusu kuondoa vikwazo vya biashara ambapo Amefafanua wamekuwa Wakizungumza mara nyingi kwamba kumekuwa na vikwazo vya biashara ambavyo tumekuwa ukiviondosha.

“Na kila tunapoondosha biashara inakuwa lakini tunakwenda tunarudi nyuma lakini kwa ukweli biashara yetu imekuwa ndani ya nchi zetu za Afrika Mashariki lakini kuna vikwazo ambavyo watendaji wetu katika maeneo mbalimbali wameviweka.

“Tumezungumza kuviondosha ili tukuze zaidi biashara ,tutengeneze soko la Afrika Mashariki na hili ndilo Rais Museven alitumia muda mrefu kulieleza soko la Afrika Mashariki.Wenzetu wa nje wanatuletea vya kwao lakini sisi wenyewe tunazalisha lakini hatuna soko, kwahiyo hilo nalo tumelizungumza kwa kiasi kikubwa.”

Wakati huo huo Rais Samia amesema katika mazungumzo yao wamezungumza kuhusu kuendelea kuzalisha nishati katika miradi ya ushirikiano ambayo inahusisha hayo mabomba lakini utekelezaji wa miradi midogo midogo itakayozalisha nidhati kwa ajili ya matumizi yetu ndani ya nchi zetu

“Lakini kama mnavyojua katika ngazi za kimataifa Tanzania na Uganda tunafanyakazi kwa karibu zaidi na hapa leo tumshukuru sana Rais wa Uganda na timu yake kwasababu mwakani Tanzania ilikuwa na Uganda tunagombania kiti cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.

“Ni zamu yetu kama Afrika Mashariki lakini nilivyomuomba Rais Museven akasema anajitoa, kwahiyo tunawashukuru sana lakini Uganda nayo inagombania kiti kama hicho ndani ya Umoja wa Afrika nasi tumeahidi tunawapa nguvu

“Jingine Rais Museven kwa sasa hivi ni Mwenyekiti wa nchi za Maziwa Makuu na kama mnavyojua ndani ya nchi za maziwa makuu usalama hauko vizuri sana…

“Hivyo anamkakati wa kuanza mazungumzo ya kuleta usalama ndani ya maziwa makuu nasi kama Tanzania tumemwambia tunamuunga mkono na tuko tayari kumsaidia atakavyoona inafaa katika jambo hili,”amesema Rais Dk.Samia

Pamoja na hayo amempongeza Rais Museven kwa kufanya ziara ya kikazi ikiwa ni siku chache baada ya kutangazwa kushinda kwa kishindo nchini Uganda na ziara hiyo imeonesha umuhimu mkubwa wa ajenda za ushirikiano kati ya Tanzania na Uganda lakini pia kwenye ukanda wetu wa Afrika Mashariki.”

Kwa upande wake Rais wa Uganda Yoweri Museven amemshukuru Rais Samia kwa kumpokea huku akielezea madhumuni ya ukombozi wa Afrika uliokuwa na mambo muhimu matatu likiwemo la kumuondoa Mkoloni ili kuwa huru.

“Baada ya uhuru ikawa kuleta neema kwa wananchi wetu na kwa enzi za sasa neema hizo ni na kuzalisha mali, bidhaa na huduma.“Hivyo unapozalisha mali au bidhaa lazima upate mtu wa kununua. Hivyo kuna haja ya kuwa na soko la uhakika katika Afrika Mashariki na Afrika kwa ujumla,”amesema Rais Museven

Pia amezungumzia umuhimu wa kuweka mkakati wa kuimarisha ulinzi na usalama ambapo amesisitiza haja ya kuwa na mkakati madhubuti wa kujihami kwa Afrika .












Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu, amesema serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan imeanza mapitio ya kuhakikisha inaweka ada elekezi zitakazotumika kwa vyama vyote vya wafanyakazi nchini ili kuondoa mkanganyiko na kuhakikisha ushindani wa haki katika uendeshaji wa vyama hivyo.

Akifungua kikao cha Baraza la Chama cha Walimu Tanzania (CWT) leo Februari 7, 2026, Jijini Dodoma, Waziri Sangu amesema serikali inalenga kuwa na vyama vinavyowajibika, na vinavyofanya mikutano kwa kuzingatia katiba za vyama pamoja na kuimarisha majadiliano kuanzia ngazi ya vijiji na matawi.

Amesema serikali tayari imeanza mapitio ya mifumo ya uendeshaji wa vyama vya wafanyakazi na itatoa maelekezo ya pamoja yatakayohakikisha vyama vyote vinafuata utaratibu mmoja wa utozaji wa ada badala ya kila chama kujipangia viwango vyake.

Ameongeza kuwa serikali inaheshimu na kuthamini mikataba ya kazi ya kimataifa, huku akisisitiza msimamo wa kuwa na vyama imara na si vyama vya mifukoni, na kwamba hatua kali za kisheria zitaendelea kuchukuliwa dhidi ya waajiri wanaokiuka sheria kwa kuruhusu vyama ambavyo havijakidhi vigezo vya kisheria kuendesha shughuli zao.

Akizungumzia malalamiko ya malimbikizo ya madeni ya walimu, amesema serikali tayari imetoa waraka wa kudhibiti madeni yaliyofanyika kiholela na kuwataka waajiri kuweka mipango ya ulipaji ili kuepusha migogoro baina ya serikali na wafanyakazi.

Kuhusu walimu wanaojiendeleza kielimu kuhesabika kama watoro kazini, Waziri Sangu amesema ofisi yake inalifanyia kazi suala hilo, akisisitiza kuwa serikali itaendelea kushirikiana na walimu kutatua changamoto zao, huku haki na wajibu vikiendelea kuzingatiwa kwa usawa.

Awali, akisoma risala ya CWT kwa mgeni rasmi, Katibu Mkuu wa chama hicho, Joseph Misalaba, amesema CWT inaiomba serikali kushughulikia changamoto ya mazingira yasiyo sawa yanayotokana na mkanganyiko wa kisheria, kanuni na miongozo, hali inayosababisha tofauti kubwa za ada kati ya chama kimoja cha wafanyakazi na kingine.

Amesema sheria zinatoa mamlaka kwa chama chenye idadi kubwa ya wanachama kubeba majukumu ya kuwatumikia watumishi katika kada husika, jambo linaloambatana na gharama kubwa za uendeshaji, uajiri wa watumishi na utetezi wa wanachama, tofauti na vyama vingine ambavyo havina wajibu huo na hivyo kutoza ada ndogo zaidi.

Kwa mujibu wa Misalaba, hali hiyo imekuwa ikiwasababisha wafanyakazi kuchagua vyama vyenye makato nafuu bila kuzingatia huduma halisi zinazotolewa, jambo linaloathiri uendeshaji wa vyama vinavyobeba majukumu makubwa kisheria.

Amesema kumekuwa na uwepo wa baadhi ya waajiri wanaoshindwa kusimamia ipasavyo sheria na kanuni kwa kuruhusu vyama kuendesha shughuli bila kukidhi masharti ya kisheria na ya kikatiba, na kuiomba Ofisi ya Waziri wa Kazi kutoa maelekezo ya wazi kwa waajiri wote nchini.

Kwa upande wa Rais wa CWT Suleiman Komba,ameipongeza serikali kwa kuendelea kuajiri walimu wapya katika shule za msingi na sekondari, huku akitoa rai ya kurejeshwa kwa posho ya kufundishia kutokana na walimu kufanya kazi kwa muda unaozidi masaa ya kawaida ya kazi, pamoja na posho za likizo zilipwe kwa wakati kwani Walimu kimsingi ni watulivu, wanaheshimu serikali na kutekeleza wajibu wao.





CHUO Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) kimeanza rasmi Awamu ya Pili ya Programu ya Msingi ya Sayansi kwa wanawake wanaotoka katika mazingira magumu kwa mwaka wa masomo 2025/2026, mkoani Singida.

Programu hiyo inayofadhiliwa na Benki ya Dunia kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET) na kuratibiwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. Lengo kuu ni kuwapatia wanawake waliokosa fursa ya awali ya kusoma masomo ya sayansi, msingi imara wa kitaaluma, kujiamini na maarifa yatakayowawezesha kuendelea na elimu ya juu pamoja na kufanikisha ndoto zao za kitaaluma.

Kupitia mafunzo hayo, washiriki wanajengewa misingi madhubuti katika masomo ya sayansi kama hatua ya maandalizi ya kuendelea na masomo ya juu katika fani za Sayansi, Teknolojia na nyanja zinazohusiana.

Akizungumza kuhusu utekelezaji wa programu hiyo, Mkurugenzi wa Taasisi ya Elimu Endelevu ya Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Dkt. Leopold Jacob Mwalongo, amesema mpango huo ni sehemu ya mkakati wa chuo katika kukuza ushiriki wa wanawake kwenye masomo ya sayansi na kuimarisha usawa wa kijinsia katika elimu.

“Programu hii inalenga kupanua fursa za elimu kwa wanawake waliokosa nafasi ya awali ya kusoma masomo ya sayansi. Kupitia mpango huu, tunachangia kujenga jamii jumuishi na kuongeza idadi ya wanawake katika fani za sayansi na teknolojia. Kwa mwaka wa masomo 2025/2026, jumla ya wanawake 247 wamefanikiwa kujiunga na kuanza mafunzo haya,” amesema Dkt. Mwalongo.

Uzinduzi wa Awamu ya Pili ya programu hii unaendelea kuonesha dhamira ya Chuo Kikuu Huria cha Tanzania ya kuendeleza elimu jumuishi na kuimarisha usawa wa kijinsia, huku ukichangia jitihada za kitaifa za kukuza rasilimali watu yenye ujuzi katika sayansi na teknolojia kwa maendeleo endelevu ya taifa.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni mara baada ya kuwasili katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 07 Februari, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni akisaini Kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 07 Februari, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha ya pamoja na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni mara baada ya kuwasili katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 07 Februari, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni mara baada ya kuwasili katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 07 Februari, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongoza ujumbe wa Tanzania kwenye mazungumzo ya pamoja na Ujumbe wa Uganda uliongozwa na Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 07 Februari, 2026. 
 


Top News