Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimkabidhi Waziri wa Idara ya Kimataifa ya Chama cha Kikomunisti cha China Mhe. Liu Haixing, Ujumbe Maalumu kwenda kwa Rais wa China Mhe. Xi Jinping mara baada ya mazungumzo, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Mei, 2026.






Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, leo tarehe 20 Mei 2026 amewasili mkoani Arusha kwa shughuli za Kikazi. Pamoja na mambo mengine Mhe. Makamu wa Rais anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika Mkutano wa 13 wa Kitaaluma wa Waandishi Waendesha Ofisi Tanzania (TAPSEA) utakaofanyika kesho tarehe 21 Mei 2026 katika Ukumbi wa Ngurdoto mkoani Arusha.



▪️Asema migogoro ya ardhi inahitaji suluhisho la kudumu la kitaasisi

▪️Asisitiza mifumo ya utatuzi wa migogoro iimarishwe

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuimarisha mifumo ya utatuzi wa migogoro ya ardhi nchini ili kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa haraka, kwa uwazi na kwa kuzingatia misingi ya utawala bora.

“Utaratibu mzuri wa utawala bora ni ule wa kitaasisi, unaowezesha wananchi kupata haki zao kupitia mifumo imara,” amesema Dkt. Nchemba.

Amesema hayo leo Jumatano, Mei 20, 2026 wakati akisikiliza na kushughulikia kero za wananchi wa maeneo ya Mahomanyika, Ndachi, Mbuyuni na Nkuhungu Broad Acres katika kikao kilichofanyika katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma.

Kikao hicho kilihusisha viongozi kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Wizara ya Katiba na Sheria, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Jiji la Dodoma pamoja na wataalamu wa ardhi kutoka ngazi mbalimbali za Serikali.

Katika kikao hicho, Waziri Mkuu alipokea taarifa za kina kuhusu hali ya migogoro ya ardhi katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dodoma pamoja na hatua zilizochukuliwa na Serikali katika kushughulikia migogoro hiyo.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema ipo haja ya kufanya mapitio ya kina ya mfumo wa mabaraza ya ardhi kutokana na mabadiliko makubwa yaliyotokea katika upatikanaji wa huduma za mahakama nchini.

Amesema wakati mfumo huo unaanzishwa, lengo lilikuwa kusogeza huduma karibu na wananchi, lakini kwa sasa mahakama zimeenea katika maeneo mengi zaidi hali inayotoa fursa ya kutathmini upya ufanisi wa mfumo huo.

Kwa upande wake, Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Juma Homera amesema tayari Serikali imeandaa hati ya mwongozo wa namna ya kushughulikia kesi za ardhi kupitia mahakama na kwamba hatua zilizobaki ni kukamilisha taratibu za uwasilishaji kwa mamlaka husika.

Naye Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Patrobas Katambi amesema ongezeko la thamani ya ardhi Jijini Dodoma baada ya Serikali kuhamia Makao Makuu limechangia kuongezeka kwa migogoro ya ardhi, uvamizi wa maeneo pamoja na biashara holela ya viwanja.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Kaspar Mmuya amesema Serikali itaendelea kushughulikia migogoro hiyo kwa kuzingatia sheria, haki na maslahi ya wananchi huku ikiendelea kulinda maeneo ya umma dhidi ya uvamizi.







Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa, akiwa katika picha ya pamoja na wawakilishi wa Shirika lisilo la Serikali la INADES pamoja na Mratibu wa Kitaifa wa Maadhimisho ya Siku ya Mnyama Punda kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Shabani Tozzo, muda mfupi baada ya ujumbe huo kufika ofisini kwake Mei 20, 2026 jijini Dodoma.
Mkurugenzi wa Shirika lisilo la Serikali la “INADES” Bi. Jacqueline Nicodemus akimkabidhi Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa tuzo ya pongezi leo Mei 20,2026 kwenye ofisi ndogo za Wizara hiyo zilizopo jengo la Kambarage jijini Dodoma kufuatia ushiriki wa Wizara yake kwenye Maadhimisho ya kitaifa ya Punda yaliyofanyika Mei 08,2026 mkoani Geita.
Mkurugenzi wa Shirika lisilo la Serikali la “INADES” Bi. Jacqueline Nicodemus akimuonesha Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa miongozo mbalimbali ya ustawi wa mnyama Punda muda mfupi baada ya kufika ofisini kwake Mei 20,2026 jijini Dodoma.
Mratibu wa kitaifa wa Maadhimisho ya siku Punda Duniani kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Shabani Tozzo (kushoto) akimkabidhi Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa tuzo ya pongezi iliyotolewa na Shirika lisilo la Serikali la INADES kwa kanda ya Afrika leo Mei 20,2026 kwenye ofisi ndogo za Wizara hiyo zilizopo jengo la Kambarage jijini Dodoma kufuatia ushirikiano uliotolewa na Wizara yake kwenye Maadhimisho hayo yaliyofanyika kitaifa Mei 08,2026 mkoani Geita.
Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa akiwa kwenye picha ya pamoja na wawakilishi wa Shirika lisilo la Serikali la “INADES” na Mratibu wa kitaifa wa Maadhimisho ya Siku ya mnyama Punda kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Shabani Tozzo muda mfupi baada ya ujumbe huo kufika ofisini kwake Mei 20,2026 jijini Dodoma.

Na Mwandishi Wetu

MAMLAKA ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) imepongeza uamuzi wa Bodi na Menejimenti ya Kampuni ya Equity For Tanzania (EFTA) kwa kutekeleza mikakati yenye lengo la kuboresha na kuimarisha utendaji wa Kampuni hiyo huku pia mauzo ya Hatifungani yake yakiwa yamepata mafanikio ya asilimia 220.24.

CMSA imeyasema hayo leo Mei 20,2026 jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya kuorodheshwa kwa toleo la kwanza la Hatifungani ya Kampuni ya Equity For Tanzania (EFTA)kwa ajili ya kuendeleza sekta ya kilimo,viwanda na biashara katika Soko la Hisa Dar es Salaam (DSE).

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), CPA.Nicodemus Mkama amesema dhamira ya Serikali ni kuona sekta ya fedha inawezesha upatikanaji wa rasilimali fedha kwa ajili ya kukuza na kuendeleza biashara zinachangia ukuaji na ustawi wa sekta binafsi, umma na uchumi wa nchi kwa ujumla.

“Hivyo Hatifungani ya EFTA imetoa mchango mkubwa katika utekelezaji wa dhamira hii, na ni hatua madhubuti ya kuongeza fursa za uwekezaji katika masoko ya mitaji na kuleta matokeo chanya kwenye uchumi wa nchi yetu.

“Kama tulivyoshuhudia mauzo ya hatifungani ya EFTA yamepata mafanikio ya asilimia 220.24, ambapo kiasi cha Sh.bilioni 33.04 kimepatikana, ikilinganishwa na Sh.bilioni 15 zilizotarajiwa.

“Hatua hii inaiwezesha EFTA kuongeza rasilimali fedha na ukwasi, ambao utatumika kutoa mikopo ya vifaa vya uzalishaji kwa Kampuni ndogo na za Kati za Ujasiriamali (SMEs), kama vile Matrekta na vifaa vya kilimo,Mashine za Kuchakata,magari ya mizigo na utalii, mitambo ya uchimbaji wa madini, vifaa vya ujenzi na mitambo ya viwandani.”

Akieleza zaidi amesema kampuni ya EFTA imeweka historia ya kuwa kampuni ya kwanza katika sekta ya fedha inayotoa huduma ya

ukodishaji wa vifaa vya uzalishaji bila dhamana kuuza hatifungani kwa umma na kupata mafanikio makubwa, na hatimaye hatifungani hiyo inaorodheshwa Soko la Hisa la Dar es Salaam.

“ Hatua hii inaweka msingi imara na inafungua milango kwa kampuni na taasisi zingine katika sekta ya umma na binafsi ambazo zinaonyesha nia ya kutumia fursa katika masoko ya mitaji kupata fedha za kuendesha biashara na kugharamia miradi ya maendeleo.

“Pia hatua hii ni sehemu ya utekelezaji wa Mkakati wa Serikali wa Njia Mbadala za Kugharamia Miradi ya Maendeleo uliowekwa kama sehemu ya utekelezaji wa Mpango Mkuu wa Maendeleo ya Sekta ya Fedha 2020/21 – 2029/30 wenye lengo la kuwezesha upatikanaji wa rasilimali fedha kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli na miradi ya maendeleo katika sekta ya umma na binafsi,”amesema CPS.Mkama.

Ameongeza kati ya wawekezaji waliowekeza kwenye hatifungani ya EFTA, asilimia 95.4 ni wawekezaji mmoja mmoja na asilimia 4.53 ni Kampuni na Taasisi.Asilimia 99.4 ni wawekezaji wa ndani wakati asilimia 0.57 ni wawekezaji wa kigeni.

Amefafanua pia kuorodheshwa kwa hatifungani ya EFTA hivi kunaongeza thamani ya uwekezaji katika Hatifungani za Kampuni na Taasisi kwa asilimia 1.66 na kufikia Sh.trilioni 2.03,

kutoka Sh.trilioni 1.99 na ushiriki huo mkubwa wa wawekezaji mmoja mmoja wa ndani ni hatua muhimu katika kuongeza ukwasi katika soko la hisa.

CPA.Mkama amesema hatua hiyo ni sehemu muhimu ya utekelezaji wa Mpango Jumuishi wa Huduma za Kifedha wenye lengo la kuongeza ushiriki wa wananchi kwenye sekta rasmi ya fedha.

“Hivyo, tuna kila sababu ya kuipongeza EFTA pamoja na taasisi na wataalamu wote walioshiriki katika kuwezesha mafanikio haya. Ninatambua kwamba, kazi hiyo haikuwa ndogo na rahisi lakini mmeweza kufanya kazi yenu vizuri.”

Wakati huo huo ametoa mwito kwa kampuni zenye leseni ya kutoa huduma katika masoko ya mitaji kuendeleza mikakati ya kuanzisha bidhaa bunifu zinazopanua na kuongeza fursa kwa wawekezaji wa ndani na wa kimataifa.

Aidha CMSA itaendelea kutekeleza na kusimamia utekelezaji wa mikakati yenye lengo la kuchagiza maendeleo ya masoko ya mitaji na hivyo kujenga uchumi shindani kwa maendeleo ya watu.













Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dennis Londo, amesema Serikali imejipanga kuhakikisha utekelezaji wa Dira ya Taifa ya mwaka 2050 unafanikiwa kupitia matumizi ya vipimo sahihi katika sekta mbalimbali za uchumi.

Akizungumza Mei 20, 2026 jijini Dodoma wakati wa maadhimisho ya Siku ya Vipimo Duniani, Londo amesema vipimo sahihi vina mchango mkubwa katika maendeleo ya biashara, kilimo na maisha ya kila siku ya wananchi.

Aidha, amesema Serikali inachukua hatua dhidi ya changamoto ya uuzaji wa mazao kwa mfumo wa “lumbesa”, ambapo watakaa pamoja na Wizara za Kilimo pamoja na TAMISEMI ili kuhakikisha mfumo huo unatokomezwa na wananchi wanazingatia matumizi ya vipimo vinavyokubalika kisheria.

Pia amesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi katika kuongeza ufanisi wa huduma na kulinda maslahi ya wananchi dhidi ya udanganyifu wa vipimo.

Kutokana na changamoto hizo, Wakala wa Vipimo kwa kushirikiana na Kampuni ya Climb Up Limited chini ya Mkurugenzi Mtendaji Emmanuel Ngallah imekuja na mfumo maalum wa mizani janja ya kidigitali unaolenga kudhibiti udanganyifu wa vipimo katika biashara mbalimbali.

Maadhimisho ya Siku ya Vipimo Duniani huadhimishwa kila mwaka Mei 20, yakilenga kuhamasisha matumizi ya vipimo sahihi kwa manufaa ya jamii na maendeleo ya uchumi.








Na Janeth Raphael MichuziTv- Bungeni Dodoma

Mbunge wa Korogwe Vijijini, Timotheo Paul Mnzava, ameitaka Serikali kuongeza kasi ya maboresho na upanuzi wa miundombinu ya barabara zinazounganisha Bandari ya Tanga na maeneo mbalimbali ya nchi, akisisitiza kuwa ufanisi wa bandari hiyo hautakuwa na maana kamili bila barabara imara za usafirishaji wa mizigo.

Akichangia mjadala wa makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Ujenzi kwa mwaka wa fedha 2026/2027 Bungeni jijini Dodoma, Mnzava amesema maboresho yanayoendelea katika Bandari ya Tanga yameongeza kiasi kikubwa cha shehena ya mizigo, hatua ambayo ni mafanikio makubwa kwa uchumi wa taifa.

Hata hivyo, amesema mafanikio hayo yanapaswa kuendana sambamba na uboreshaji wa barabara kuu zinazopeleka mizigo kutoka bandari hiyo kwenda maeneo mbalimbali ya nchi, ili kuhakikisha ufanisi wa huduma na kupunguza gharama za usafirishaji.

“Uwekezaji mkubwa uliofanyika kwenye Bandari ya Tanga unapaswa kuendana na uboreshaji wa barabara. Bila hivyo, tunapoteza maana ya maendeleo haya,” amesema Mnzava.

Ameeleza kuwa baadhi ya barabara muhimu katika mtandao huo zimechoka na zimepitwa na muda wa matumizi yake, huku Serikali ikiwa imekuwa ikitoa ahadi za kuzifanyia matengenezo kwa muda mrefu bila utekelezaji wa haraka unaotarajiwa.

Aidha, amemtaka Waziri wa Ujenzi kufafanua kwa kina mikakati ya Serikali kuhusu upanuzi na ukarabati wa barabara ya Tanga–Segera pamoja na Segera–Chalinze, ambazo ni njia muhimu zinazounganisha mikoa ya Kaskazini na maeneo mengine ya nchi.

Mnzava amesema barabara hizo si tu za kiuchumi kwa mikoa ya Kaskazini, bali zinahudumia Watanzania wengi kutoka maeneo mbalimbali ikiwemo Tanga, Morogoro, Singida na Dodoma, ambao wanategemea miundombinu hiyo kwa shughuli za usafirishaji wa mizigo na biashara.

Ameongeza kuwa ili barabara hizo ziweze kutimiza lengo la kuongeza ufanisi wa Bandari ya Tanga, ni lazima Serikali iweke wazi hatua zilizochukuliwa na muda wa utekelezaji wa miradi hiyo muhimu ya kimkakati.

“Ni muhimu Serikali kueleza wazi hatua zilizofikiwa na mipango ya muda mfupi na mrefu kuhusu ujenzi na upanuzi wa barabara hizi,” amesisitiza.

Katika hitimisho lake, Mnzava ametoa wito kwa wananchi wa maeneo yanayonufaika na barabara hizo kushirikiana pamoja katika kuunga mkono maendeleo ya miundombinu hiyo, akisema ni chachu ya ukuaji wa uchumi na ustawi wa taifa kwa ujumla.





Farida Mangube Morogoro
JESHI la Polisi Mkoa wa Morogoro linawashikilia watu wawili, Bashiri Abdallah Matenga (22), dereva bodaboda mkazi wa mtaa wa Bomba la Zambia, kata ya Kingolwira Manispaa ya Morogoro, pamoja na Gabriel Daniel Issaya (26), dereva bodaboda mkazi wa Mkambarani wilayani Morogoro, kwa tuhuma za kuhusika na mauaji ya Brian Emanuel Mkilya (22), mkazi wa Mkoa wa Mara aliyekuwa akiishi kata ya Mkambarani wilayani Morogoro.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na jeshi hilo, imesema tukio hilo lilitokea Mei 17, 2026 majira ya saa 5 asubuhi katika eneo la Kingolwira, Manispaa ya Morogoro. Inadaiwa kuwa marehemu alishambuliwa na kundi la watu waliokuwa wamejichukulia sheria mkononi wakimtuhumu kuiba pikipiki.

Watuhumiwa ambao wote ni madereva bodaboda na wakazi wa Morogoro, wanaendelea kuhojiwa huku uchunguzi wa tukio hilo ukiendelea ambapo Polisi wamesema hatua za kisheria zitachukuliwa mara baada ya upelelezi kukamilika.

Katika taarifa yake, Jeshi la Polisi limeonya wananchi dhidi ya tabia ya kujichukulia sheria mkononi, likieleza kuwa vitendo hivyo vinaweza kusababisha madhara makubwa ikiwemo kupoteza maisha na kujeruhi watu wasiokuwa na hatia.

Aidha, wananchi wametakiwa kutoa taarifa kwa vyombo vya usalama pindi wanapohisi kuwepo kwa vitendo vya uhalifu ili sheria iweze kuchukua mkondo wake.

Na Mwandishi Wetu
MKURUGENZI Mkuu wa Taasisi ya Elimu Tanzania (TET), Dkt. Aneth Komba, amezitaka taasisi za elimu ya juu nchini kuhakikisha tafiti, ubunifu pamoja na matumizi ya teknolojia vinaelekezwa katika kutoa suluhisho la changamoto halisi zinazowakabili wananchi na kuchochea maendeleo ya taifa.

Dkt. Komba alisema hayo wakati akifungua Maadhimisho ya Wiki ya 11 ya Utafiti na Ubunifu katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Kishiriki cha Elimu (DUCE), yaliyowakutanisha wanafunzi, wahadhiri, watafiti, wabunifu pamoja na wadau mbalimbali wa elimu na maendeleo.

Aidha, alieleza utayari wake wa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Kishiriki cha Elimu (DUCE), Taasisi ya Global Education Link (GEL) pamoja na wadau wengine wa elimu nchini katika kuimarisha mwongozo wa taaluma kwa wanafunzi na walimu ili kuwaandaa vijana kuendana na mahitaji ya dunia ya sasa na ya baadaye.

Utayari huo umeelezwa na Dkt. Komba wakati alipotembelea banda la Global Education Link katika maadhimisho hayo, ambapo alisema changamoto ya mwongozo wa taaluma imekuwa kubwa nchini huku akisisitiza kuwa maandalizi ya mwanafunzi kuhusu mustakabali wake yanapaswa kuanza mapema tangu akiwa shule ya msingi.

Alisema maendeleo ya taifa hayawezi kupatikana bila uwekezaji mkubwa katika elimu, tafiti, ubunifu, teknolojia na ushirikishwaji wa jamii, huku akisisitiza kuwa elimu bora haipaswi kuishia darasani pekee bali iwe nyenzo ya kutatua changamoto za kijamii na kiuchumi.

“Tafiti na ubunifu vinapaswa kuwa na manufaa ya moja kwa moja kwa jamii. Tusifanye tafiti ambazo zinaishia kwenye makabati, bali tafiti zinazotoa majibu ya changamoto za wananchi,” alisema Dkt. Komba.

Alisema kuwa katika dunia ya sasa matumizi ya teknolojia na mifumo ya kidijitali ni muhimu katika kuongeza ufanisi wa kazi, kuboresha huduma kwa jamii pamoja na kuharakisha maendeleo katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu, uchumi, mazingira, usafiri na afya.

Dkt. Komba alisema pia kuna umuhimu mkubwa wa kuwajengea uwezo walimu waliopo mashuleni ili wawe sehemu ya mfumo wa kuwaelekeza wanafunzi katika uchaguzi sahihi wa taaluma.

“Tunapaswa kuhakikisha watoto wanaelewa mapema wanataka kufanya nini katika maisha yao. Akishafanya maamuzi yasiyo sahihi katika hatua za awali inaweza kuwa changamoto kubwa baadaye,” alisema.

Kaimu Mkuu wa DUCE, Prof. Amani Lusekelo, alisema hadi sasa jumla ya tafiti 45 zimefanyika kupitia programu ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu na baadhi yake tayari zimeanza kutumiwa na halmashauri mbalimbali nchini katika kuboresha huduma za kijamii na elimu.

Prof. Lusekelo alisema maadhimisho hayo yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kuonesha kazi za watafiti na wabunifu pamoja na kuimarisha ushirikiano kati ya vyuo vikuu, serikali, sekta binafsi na jamii katika kutatua changamoto mbalimbali.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Global Education Link, Abdulmalik Mollel, alisema bado kuna changamoto kubwa ya wanafunzi wengi kuchagua taaluma kwa kufuata mitazamo ya kijamii badala ya kuzingatia mahitaji halisi ya ajira na maendeleo ya dunia ya sasa.

Alisema tafiti walizozifanya katika shule mbalimbali zinaonesha kuwa zaidi ya asilimia 90 ya wanafunzi wa masomo ya sayansi, hususan PCB, wanataka kusomea udaktari huku kada nyingine muhimu zikiwa na uhaba mkubwa wa wataalamu.

“Tunawakuta wanafunzi wengi wa PCB wanataka kuwa madaktari, lakini ukiangalia mahitaji ya sasa kuna maeneo kama radiology, physiotherapy, audiology, speech therapy, dialysis na dentistry yenye uhitaji mkubwa wa wataalamu lakini wanafunzi hawapelekwi huko kwa sababu hawapati mwongozo sahihi wa taaluma,” alisema Mollel.

Kaulimbiu ya Wiki ya 11 ya Utafiti na Ubunifu DUCE mwaka huu imejikita katika matumizi bora ya rasilimali za madini nchini kwa ajili ya kuendeleza nishati jadidifu, mabadiliko ya kidijitali pamoja na kuimarisha usalama wa jamii.

Washiriki wa maadhimisho hayo pia walipata fursa ya kuonesha bunifu mbalimbali za kiteknolojia pamoja na tafiti zinazolenga kutatua changamoto zinazoikabili jamii katika sekta mbalimbali.



Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) imezindua rasmi mfuko maalumu wa kuchangia huduma za matibabu ya kibingwa na ubingwa bobezi, ukiwa na lengo la kuimarisha upatikanaji wa matibabu ya upandikizaji viungo nchini, huku mafanikio makubwa yakiripotiwa kwa watoto 30 waliopandikizwa uloto na kupona.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa BMH, Profesa Abel Makubi, amesema uanzishwaji wa mfuko huo umetokana na ongezeko la mahitaji ya huduma za upandikizaji viungo pamoja na uhitaji wa kushirikisha wadau mbalimbali katika kuunga mkono jitihada za serikali.

Profesa Makubi ameeleza kuwa hospitali hiyo imepiga hatua kubwa katika huduma za kibingwa, ambapo upandikizaji wa figo ulianza mwaka 2018 na hadi sasa wagonjwa 56 tayari wamenufaika kwa mafanikio makubwa.

Aidha, amesema huduma ya upandikizaji wa uloto ilianza mwaka 2023 na hadi sasa watoto 30 wamefanyiwa upasuaji huo na wote wanaendelea vizuri kiafya, hatua inayoonesha maendeleo makubwa ya tiba za kibobezi nchini.

Ameongeza kuwa mfuko huo utasaidia si tu wagonjwa wanaosubiri matibabu, bali pia kupanua miundombinu na kuboresha huduma za kibingwa ili kufikia wagonjwa wengi zaidi.

Katika hatua nyingine, Profesa Makubi amebainisha kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imechangia Shilingi bilioni 1 kusaidia huduma hizo, huku akisisitiza umuhimu wa wadau wengine kuendelea kushiriki.

WITO WA USHIRIKIANO KUIMARISHA HUDUMA ZA FIGO NA SIKOSELI

Kwa upande wake, Naibu Spika Daniel Sillo amesema ushiriki wa wananchi, taasisi na wadau binafsi ni muhimu katika kuimarisha huduma za matibabu ya magonjwa sugu ikiwemo figo na sikoseli.

Amesema gharama za matibabu ya kibingwa bado ni kubwa, hivyo haziwezi kubebwa na serikali pekee, jambo linalohitaji mshikamano mpana wa jamii nzima.

Akizungumza katika hafla ya chakula cha jioni kilichowakutanisha viongozi na wadau wa afya, Sillo amesema michango ya hiari inaweza kusaidia kuokoa maisha ya wagonjwa wengi wanaohitaji upandikizaji na matibabu maalumu.

Ameongeza kuwa magonjwa hayo hayabagui mtu kwa nafasi, kipato au hali ya maisha, hivyo ni jukumu la pamoja kuhakikisha kila mwenye uhitaji anapata matibabu kwa wakati.

Sillo amesisitiza kuwa kuongezeka kwa michango kutasaidia pia kuboresha miundombinu ya afya na kuongeza uwezo wa hospitali kutoa huduma za kibingwa ndani ya nchi badala ya wagonjwa kusafirishwa nje kwa gharama kubwa.

Kwa ujumla, jitihada hizo za BMH pamoja na wito wa wadau zinaendelea kuonesha mwelekeo chanya wa Tanzania kupunguza utegemezi wa matibabu ya nje na kuimarisha huduma za kibingwa ndani ya nchi.









Na Janeth Raphael MichuziTv- Bungeni Dodoma.

Mbunge wa Kibakwe, George Simbachawene, amesema kuwa maendeleo makubwa yanayoendelea kufanyika katika Jiji la Dodoma hayapaswi kutafsiriwa kama upendeleo wa Serikali kwa mkoa huo, bali ni utekelezaji wa wajibu wa kitaifa kutokana na hadhi ya Dodoma kuwa makao makuu rasmi ya nchi.

Simbachawene ameyasema hayo leo bungeni jijini Dodoma wakati akichangia hoja ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Ujenzi kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Katika mchango wake, mbunge huyo alisema kumekuwepo na maneno pamoja na minong’ono kutoka kwa baadhi ya watu wakidai kuwa Dodoma inapendelewa kwa kupewa fedha nyingi na miradi mikubwa ya maendeleo ikilinganishwa na maeneo mengine ya Tanzania.

Hata hivyo, Simbachawene amesisitiza kuwa hoja hizo hazina msingi, akieleza kuwa Dodoma ni makao makuu ya Watanzania wote na si mali ya kundi, mkoa au eneo fulani pekee.

“Dodoma ni makao makuu ya nchi. Ni ya Watanzania wote. Hatuwezi kuizungumza Dodoma kana kwamba ni eneo la watu wachache au linafanyiwa upendeleo maalum,” alisema Simbachawene bungeni.

Alifafanua kuwa uamuzi wa kuhamishia shughuli za Serikali pamoja na hadhi ya makao makuu ya nchi kwenda Dodoma ulifanywa kwa mujibu wa sheria na maamuzi ya kitaifa yaliyolenga kuijenga Tanzania kwa usawa na ufanisi mkubwa wa kiutawala.

Kwa mujibu wa Simbachawene, sheria hiyo iliyopitishwa miaka ya nyuma ndiyo iliyoweka msingi wa Dodoma kupewa hadhi maalum ya kuwa kitovu cha utawala wa nchi, hivyo ni jambo la kawaida kwa Serikali kuelekeza nguvu kubwa katika ujenzi wa miundombinu, barabara, taasisi pamoja na huduma mbalimbali muhimu katika jiji hilo.

Amesema nchi nyingi duniani huwekeza kwa kiwango kikubwa katika miji yao ya makao makuu ili kuhakikisha inakuwa mfano wa maendeleo, utawala bora na utoaji wa huduma, hivyo Tanzania nayo haina budi kufanya hivyo kwa Dodoma.

Mbunge huyo ameongeza kuwa kazi kubwa inayofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Samia Suluhu Hassan katika kuibadilisha Dodoma itaendelea kukumbukwa katika historia ya taifa.

Alieleza kuwa maendeleo yanayoonekana sasa katika sekta ya miundombinu, hususan barabara na huduma za kijamii, ni sehemu ya safari ya kuifanya Dodoma kuwa jiji la kisasa linaloakisi hadhi ya Tanzania kama taifa.

“Historia itaandika kazi kubwa inayofanyika Dodoma. Hii ni kazi ya kizalendo na ya kutukuka kwa manufaa ya Watanzania wote,” aliongeza.

Simbachawene pia aliwataka Watanzania kuangalia maendeleo ya Dodoma kama uwekezaji wa kitaifa wenye manufaa mapana kwa nchi nzima, badala ya kuyaona kama kipaumbele kinachowanyima haki wananchi wa maeneo mengine.

Amesisitiza kuwa maendeleo ya makao makuu ya nchi yana mchango mkubwa katika kukuza uchumi, kuboresha utendaji wa Serikali na kuimarisha taswira ya taifa ndani na nje ya Tanzania.


Mkoa wa Geita umeanzisha mradi mkubwa wa ujenzi wa ghala la madawa katika Halmashauri ya Chato, ambalo linatarajiwa kuhudumia mikoa ya Kagera, Shinyanga na Kigoma mara litakapokamilika. 

Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua miradi ya maendeleo Wilayani Chato, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Martin Shigela, alisema jengo hilo linagharimu zaidi ya shilingi bilioni 19. Ghala hilo lina ukubwa wa mita za mraba 5,000 na litahifadhi madawa pamoja na vifaa tiba kwa ajili ya vituo vya afya katika mikoa mitatu ya jirani.

Mradi huo unatekelezwa na Taasisi ya Serikali ya Medical Stores Department, MSD, na unahusisha ujenzi wa ghala pamoja na ofisi za utawala. Kwa mujibu wa mkandarasi wa mradi, Patric Laibo, ujenzi ulianza Agosti 20, 2025 na umefikia asilimia 57. Anatarajia kukamilisha kazi hiyo ifikapo Oktoba 19 mwaka huu.

Viongozi mbalimbali wameipongeza Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuwaletea huduma hiyo wananchi wa Chato na mikoa jirani. Wamesema awali wananchi walilazimika kusafiri umbali mrefu kutafuta madawa kila yanapokuwa yameisha.




 NMB Bank Plc imeweka rekodi mpya katika sekta ya benki nchini baada ya kupendekeza gawio la takribani Sh bilioni 305 kwa mwaka wa fedha wa 2025, likiwa ni sawa na Sh 610.15 kwa kila hisa. Gawio hilo linatajwa kuwa kubwa zaidi kuwahi kutangazwa na benki hiyo na miongoni mwa malipo makubwa ya gawio katika historia ya sekta ya fedha nchini.

Kiwango hicho kinajumuisha gawio la kawaida la Sh 504.26 kwa kila hisa pamoja na gawio maalumu la Sh 105.89 kwa kila hisa, ambalo ni la kwanza katika historia ya NMB. Mapendekezo hayo yanatarajiwa kuwasilishwa kwa wanahisa katika Mkutano Mkuu wa 26 wa Mwaka utakaofanyika Juni 10, 2026, katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam. 

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki hiyo, David Nchimbi, amesema kiwango hicho kinaifanya 2025 kuwa mwaka wa kihistoria kwa benki na sekta ya fedha nchini, huku, Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu, Ruth Zaipuna, amesema mafanikio hayo yametokana na utekelezaji thabiti wa Mpango Mkakati wa mwaka 2021 hadi 2025, uwekezaji katika teknolojia, maendeleo ya wafanyakazi na upanuzi wa huduma za fedha za kidijitali. Benki hiyo ilitangaza faida kabla ya kodi ya Sh trilioni 1.1, huku faida baada ya kodi ikifikia Sh bilioni 756 baada ya kukamilika kwa ukaguzi wa nje.

Ndani ya miaka mitano, jumla ya gawio la NMB imepanda kutoka Sh bilioni 48 mwaka 2020 hadi zaidi ya Sh bilioni 305 mwaka 2025, huku bei ya hisa ikiongezeka kutoka takribani Sh 2,340 hadi Sh 13,130. Hatua hiyo imeendelea kuimarisha nafasi ya NMB kama moja ya taasisi kubwa na zenye thamani kubwa zaidi za kifedha katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa NMB Bank Plc, David Nchimbi (katikati), Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu wa NMB Bank Plc, Ruth Zaipuna (kulia), na Mkurugenzi wa Uhusiano wa Wawekezaji, Uendelevu na Mawasiliano Innocent Yonazi (kushoto), wakizungumza na waandishi wa habari kuhusu mapendekezo ya gawio la rekodi la Sh bilioni 305.08 kwa mwaka wa fedha wa 2025. Gawio hilo la Sh 610.15 kwa kila hisa linatarajiwa kuwasilishwa kwa wanahisa kwa ajili ya kuidhinishwa katika Mkutano Mkuu wa 26 wa Mwaka unaotarajiwa kufanyika Juni 10











Top News