Na Mashaka Mhando, Tanga
JESHI la Polisi Mkoa wa Tanga linafanya uchunguzi wa ajali mbaya ya barabarani iliyosababisha kifo cha mgonjwa mmoja na kujeruhi watu wengine wanne, baada ya gari la wagonjwa (Ambulance) kugongana uso kwa uso na lori la mizigo.
Tukio hilo limetokea leo Machi 1, 2026, majira ya saa 6:10 usiku katika eneo la Saruji, Wilaya ya Tanga, kwenye barabara kuu ya Tanga kuelekea Segera.
Chanzo cha Ajali
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, ACP Almachius Mchunguzi, ilisema kuwa uchunguzi wa awali umebaini kuwa ajali hiyo imetokana na uzembe wa dereva wa gari la wagonjwa.
Inadaiwa kuwa dereva huyo alikuwa katika mwendo kasi uliompelekea kushindwa kulimudu gari hilo na kuhama upande wake wa kushoto na kuingia upande wa kulia, kisha kugongana uso kwa uso na lori.
Waliohusika na Madhara
Gari la wagonjwa lenye namba za usajili STM 7202, mali ya Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe, lilikuwa likitokea Mombo kuelekea Hospitali ya Rufaa ya Bombo likiendeshwa na Alphonce Alfan.
Gari hilo liligongana na lori aina ya Scania (T 628 DSG) lililokuwa likitokea Tanga kuelekea Arusha likiendeshwa na John Philipo.
Katika ajali hiyo, mgonjwa aliyekuwa akisafirishwa, Zaharia Abrahaman Mdoe (41), mkazi wa Goha – Korogwe, amepoteza maisha.
Watu wengine wanne waliojeruhiwa na kukimbizwa Hospitali ya Rufaa ya Bombo kwa matibabu ni:
Zainabu Abrahaman Mdoe
Seleman Hassan Mdoe
Naiman Msofe Mdoe Hatibu Deusi Hatibu (Muuguzi aliyekuwa akimsindikiza mgonjwa).
Onyo la Polisi
Jeshi la Polisi limetoa wito mkali kwa madereva wote nchini kuzingatia sheria za usalama barabarani na kuepuka mwendo kasi pamoja na maamuzi hatarishi wanapokuwa barabarani.
"Tunawakumbusha watumiaji wote wa barabara kuwa usalama ni jukumu la kila mmoja," ilieleza sehemu ya taarifa hiyo kutoka kwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga.
Mwili wa marehemu umehifadhiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Bombo kwa ajili ya uchunguzi wa kitatibu na taratibu nyingine za kifamilia.