WIZARA ya Uchukuzi kwa kushirikiana na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) Jumapili April 20, 2026 wamekutana na wadau mbalimbali kuzungumzia mipango ya mradi wa ujenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Serengeti ambao unatajwa kuwa miongoni mwa miradi mikubwa ya kimkakati itakayobadilisha taswira ya sekta ya usafiri wa anga na utalii nchini Tanzania.

Kikao hicho kilifanyika katika Mugumu ofisi za Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti, mkoani Mara, kikilenga kujenga uelewa wa pamoja kuhusu maendeleo na hatua za utekelezaji wa mradi huo mkubwa unaotarajiwa kuimarisha sekta ya usafiri wa anga pamoja na kukuza utalii nchini.

Mradi huo unalenga kuongeza uwezo wa kupokea ndege za kimataifa moja kwa moja, hatua itakayorahisisha upatikanaji wa watalii pamoja na wawekezaji, na hivyo kukuza uchumi wa taifa

Katika kikao hicho walikuwepo pia PSSSF, uongozi wa Halmashauri ya Serengeti pamoja na kampuni ya Saba Engineering, ambayo ni mshauri elekezi anayesimamia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa mradi huo.

Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Mkurugenzi wa Miundombinu, Bw. Shomari Shomari, amesema Wizara inatambua umuhimu wa mradi huo na imejipanga kuhakikisha unatekelezwa kwa wakati kama ulivyopangwa.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa TAA, Bw. Abdul Mombokaleo, amesisitiza kuwa mradi huo ni kichocheo muhimu cha ukuaji wa uchumi wa taifa, hasa katika kukuza utalii wa Hifadhi ya Serengeti, ambayo ni moja ya vivutio vikuu duniani. Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuzingatia masuala ya kijamii na kimazingira ili kuhakikisha wananchi wa maeneo husika wananufaika ipasavyo na mradi huo.

Hifadhi ya Taifa ya Serengeti iko kaskazini mwa Tanzania, ikienea kwa kiasi kikubwa katika Mkoa wa Mara, huku sehemu zake zikigusa pia mikoa ya Simiyu na Arusha.

Hifadhi hii ni maarufu duniani kwa uhamaji mkubwa wa wanyama, hususan zaidi ya nyumbu milioni 1.5 wanaohama kila mwaka wakifuatiwa na pundamilia na swala. Serengeti pia ni eneo la Urithi wa Dunia la UNESCO, na ni moja ya vivutio vikuu vya utalii nchini, likivutia wageni kutoka kote duniani kutokana na wingi na utofauti wa wanyamapori wake.






Chuo cha Usafiri wa Anga (CATC) kwa niaba ya Shirika la Kimataifa la Usafiri wa Anga (ICAO) kimezindua rasmi mafunzo ya Vihatarishi katika Usafiri wa Anga (Risk Management Course) tarehe 20 Aprili 2026 jijini Dar es Salaam. Mafunzo haya ya siku tano yanawakutanisha washiriki 20 kutoka Tanzania, Uganda na Eswatini wakiwawakilisha mamlaka za viwanja vya ndege na mashirika ya ndege.

Lengo la mafunzo haya ni kuwajengea washiriki uwezo wa kutambua, kuchambua na kudhibiti vihatarishi vya kiusalama katika sekta ya usafiri wa anga, sambamba na kuimarisha utekelezaji wa viwango vya kimataifa vya usalama na kukuza ushirikiano wa kikanda.

Akizungumza wakati wa ufunguzi, Mkuu wa Chuo, Bw. Aristid Kanje, alisisitiza umuhimu wa mafunzo hayo katika kuimarisha usalama wa anga kikanda, akisema:

“ICAO imeweka viwango, sisi tunatekeleza. Mafunzo haya ya Vihatarishi katika Usafiri wa Anga (Risk Management Course) ni hatua muhimu katika kujenga ukanda wa anga unaotegemewa.”

Kwa upande wake, Mkufunzi wa CATC, Bi. Christine Bugoya, alielezea umuhimu wa mafunzo hayo kwa kina, akibainisha kuwa yatawaongezea washiriki mbinu za kitaalamu za usimamizi wa vihatarishi pamoja na kuboresha kwa mapana ushirikiano wa kiusalama baina ya nchi shiriki, hali itakayochangia kubadilishana uzoefu na kuimarisha mifumo ya usalama wa anga.

Kupitia mafunzo haya, Chuo cha Usafiri wa Anga (CATC) kinaendelea kuonesha dhamira yake ya kutoa mafunzo yenye viwango vya kimataifa na kuchangia kikamilifu katika kuimarisha usalama, ufanisi na maendeleo endelevu ya sekta ya usafiri wa anga kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Usafiri wa Anga (ICAO).
Mkuu wa Chuo cha Usafiri wa Anga (CATC), Aristid Kanje akifungua mafunzo ya Vihatarishi katika Usafiri wa Anga (Risk Management Course)  yaliyoanza tarehe 20 Aprili 2026 katika chuo hicho jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya Walimu pamoja na washiriki wa Mafunzo kutoka Tanzania, Uganda na Eswatini wakiwawakilisha mamlaka za viwanja vya ndege na mashirika ya ndege wakifuatilia hotuba ya mgeni rasmi wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya Vihatarishi katika Usafiri wa Anga (Risk Management Course)
Picha ya pamoja 


Na Vero Ignatus

BENY Israel Mwaisaka, mchungaji wa kanisa la FPCT Komwale lililopo nje kidogo ya mji wa Handeni, wilaya ya Handeni mkoani Tanga anasema kuwa ninatambua na kuthamini   Amani ambayo imekwepo tangu nchi ipate uhuru imekuwa msingi mkubwa wa maendeleo limewezesha wananchi kuishi kwa utulivu na kufanya shughuli zao bila hofu.

Kupitia amani hii, Watanzania wameweza kushiriki shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi kwa uhuru mkubwa. Michezo, biashara, elimu na ibada vimekuwa vikifanyika kwa utulivu mkubwa,vilevile Vijana wamepata nafasi ya kusoma na kujiendeleza, huku watu wa dini mbalimbali wakifanya ibada zao kwa uhuru. 

Haya yote ni matokeo ya juhudi za waasisi wa taifa letu ambao waliweka msingi wa umoja, mshikamano na upendo miongoni mwa Watanzania.

Mch.Mwaisaka anasema Amani ikikosekana hali hiyo huleta hofu kwa wananchi na kuhatarisha maendeleo katika sekta mbalimbali kama vile elimu, uchumi na hata uhuru wa kuabudu hivyo Ni muhimu kutambua kuwa amani si jambo la kudumu bila jitihada, bali inahitaji kulindwa na kila mmoja wetu kwa nguvu zote.

Katika mazungumzo mbalimbali ya kijamii, ndugu Hendry Lema, ambaye ni mzee mstaafu wa kanisa la KKKT Usharika wa Engarenaro Arusha, amekuwa akisisitiza umuhimu wa amani kwa maendeleo ya taifa. Anasema kuwa amani ndiyo nguzo kuu inayowezesha jamii kustawi, na bila amani hakuna maendeleo ya kweli yanayoweza kupatikana. 

"Mimi ni baba na Kichwa cha familia pia ni mlezi wa kiroho na mshauri wa jamii, nahimiza  watu kurejea katika misingi ya upendo, heshima na kuvumiliana, 

Ni wajibu wa kila Mtanzania kuhakikisha kuwa tunadumisha misingi hii ya upendo na mshikamano. Kama alivyotuasa hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, upendo ni silaha kubwa inayoweza kuondoa chuki, ubaguzi na migogoro.

 Tukizingatia hilo, tutaweza kujenga taifa lenye umoja na lenye kuheshimiana kati ya wananchi na viongozi wao, tutangulize utu ili kuepusha migongano isiyo ya lazima.

Mwisho, nitoe wito kwa Watanzania wote bila kujali dini au imani zao, kuendelea kuliombea taifa letu na kumtanguliza Mungu katika kila jambo. Tukiwa na moyo wa toba na unyenyekevu, 

Mungu atatusaidia kulinda amani yetu na kutujalia haki ya kweli. Kama ilivyoandikwa katika Mithali 14:34, “Haki huinua taifa; bali dhambi ni aibu ya watu wote.” Mungu ibariki Tanzania, Mungu tubariki Watanzania.

BENY Israel Mwaisaka, mchungaji wa kanisa la FPCT Komwale lililopo nje kidogo ya mji wa Handeni mkoani Tanga

 

Serikali imesisitiza umuhimu wa michezo kwa wafanyakazi kama sehemu muhimu ya kuimarisha afya na kuongeza ufanisi mahali pa kazi.

Wito huo umetolewa na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe.Rahma Kisuo, wakati akifungua rasmi Michezo ya Mei Mosi Kitaifa 2026 iliyofanyika Aprili 20, 2026 katika viwanja vya Sabasaba mkoani Njombe.

Amesema kuwa afya ya mfanyakazi ni mtaji mkubwa unaochangia maendeleo ya taasisi na taifa kwa ujumla, hivyo michezo inapaswa kupewa kipaumbele.

Aidha, Mhe.Kisuo amehimiza wafanyakazi kote nchini kujenga utamaduni wa kufanya mazoezi mara kwa mara badala ya kusubiri vipindi vya mashindano pekee. Amesisitiza kuwa mazoezi yawe sehemu ya maisha ya kila siku ili kuboresha afya na kuongeza tija kazini, huku akizitaka taasisi zote za umma na binafsi kuhakikisha zinatoa nafasi kwa wafanyakazi kushiriki shughuli za michezo.

Kwa upande wake Katibu Tawala wa mkoa wa Njombe Dkt. Stephane Nindi akimwakilisha Mkuu wa mkoa wa Njombe Mhe. Anthony Mtaka amesema kuwa, kufanyika kwa Maadhimisho ya Meimosi Njombe kumetoa fursa za kibiashara kwa wananchi wa mkoa huo.

Katika hatua nyingine, amewapongeza washiriki wa Michezo ya Mei Mosi na kuwataka kudumisha nidhamu, mshikamano na ushindani wa haki.

Amesisitiza kuwa michezo iwe chachu ya kuimarisha udugu na ushirikiano miongoni mwa wafanyakazi badala ya kuwa chanzo cha migogoro.

Kwa mwaka 2026, michezo hiyo inaongozwa na kauli mbiu isemayo, “Kazi zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050,” huku watumishi na wachezaji wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC) wakiwa miongoni mwa washiriki wa ufunguzi huo.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Mlezi wa Mtandao wa Wanawake Viongozi Afrika (AWLN) Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Liberia Mhe. Ellen Johnson Sirleaf mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 20 Aprili, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Mwanachama wa Mtandao wa Wanawake Viongozi Afrika (AWLN) Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Shirikisho la Kidemokrasia la Ethiopia Mhe. Sahle - Worke Zewde mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 20 Aprili, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Uongozi wa Mtandao wa Wanawake Viongozi Afrika (AWLN) uliongozwa na Mlezi wake Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Liberia Mhe. Ellen Johnson Sirleaf, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 20 Aprili, 2026.







Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza jambo na Mlezi wa Mtandao wa Wanawake Viongozi Afrika (AWLN) Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Liberia Mhe. Ellen Johnson Sirleaf pamoja na Mwanachama wa Mtandao huo, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Shirikisho la Kidemokrasia la Ethiopia Mhe. Sahle - Worke Zewde mara baada ya mazungumzo yao, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Aprili, 2026.






 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Uongozi wa Mtandao wa Wanawake Viongozi Afrika (AWLN), uliongozwa na Mlezi wake Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Liberia Mhe. Ellen Johnson Sirleaf pamoja na Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Shirikisho la Kidemokrasia la Ethiopia Mhe. Sahle - Worke Zewde, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Aprili, 2026.







Top News