Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ameishauri Wizara ya Mambo ya Ndani kuimarisha mfumo wa utoaji wa viza kwa njia ya kidigitali ili huduma hiyo ipatikane kwa haraka kwa wageni wanaoingia nchini.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 24 Aprili 2026, alipokutana na Waziri wa Mambo ya Ndani wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Patrobas Katambi, aliyefika Ikulu Zanzibar kwa ajili ya kujitambulisha.

Rais Dkt. Mwinyi amesema kuwa kwa muda mrefu kumekuwepo na tatizo la upatikanaji wa viza kupitia mfumo wa mtandao (online), jambo linalolalamikiwa na watalii wengi wanaoingia nchini na kusababisha kutumia muda mrefu kupata huduma hiyo katika viwanja vya ndege.

Amefahamisha kuwa hatua hiyo itaongeza ufanisi na kudhibiti upotevu wa fedha unaotokana na matumizi ya fedha taslimu. 

Amesisitiza kuwa kuwepo kwa mfumo wa kidigitali ni suala la lazima katika utoaji wa viza, na kuitaka Wizara kuchukua hatua za haraka kuondoa tatizo hilo.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amesema kuwa suala jingine linalopaswa kupewa kipaumbele na Idara ya Uhamiaji ni uwajibikaji katika viwanja vya ndege, pamoja na kuimarisha utoaji wa huduma kwa haraka kwa kuwa na nguvu kazi ya kutosha muda wote na kuwajibika kwa ufanisi zaidi.

Sambamba na hilo, Rais Dkt. Mwinyi amesisitiza kwa Jeshi la Polisi kuimarisha usalama katika maeneo ya utalii ili kudhibiti matukio ya uhalifu, pamoja na kuongeza juhudi za kufanya uchunguzi wa haraka pale matukio yanapotokea na kuweka utaratibu mzuri wa utoaji wa taarifa kwa umma.

Akizungumzia suala la usalama barabarani, amesema juhudi za ziada zinahitajika kuimarisha utekelezaji wa sheria za usalama barabarani kutokana na kutofuatwa kikamilifu kwa sheria hizo, hali inayochangia ongezeko la ajali za barabarani. 

Pia amesisitiza kuimarishwa kwa juhudi za kupambana na udhalilishaji wa kijinsia, tatizo alilolieleza kuwa ni kubwa hapa nchini.

Naye Waziri wa Mambo ya Ndani, Mhe. Patrobas Katambi, amemuhakikishia Rais Dkt. Mwinyi kuwa Wizara hiyo itaendelea kutekeleza majukumu yake kwa utii na uaminifu, kwa kuzingatia Katiba, sheria na sera za nchi, na ameahidi kuyapokea na kuyafanyia kazi maelekezo yote yaliyotolewa kama dira ya utekelezaji.











Viongozi wa vyama vya ushirika mkoani Geita wametakiwa kusimamia maadili kwa dhati ili kuhakikisha wadau, hususan wakulima wadogo, wanapata haki na stahiki zao kwa wakati. 

Agizo hilo limetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Geita, Mhe. Hashim Komba, kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhe. Martin Shigela, wakati wa kilele cha Jukwaa la 4 la Maendeleo ya Ushirika mkoani humo lililofanyika Aprili 22 mwaka huu.

Katika hotuba yake, Mhe. Komba amezitaka AMCOS mbalimbali kuhakikisha zinawalipa wadau madeni yao kila msimu unapoisha. Alibainisha kuwa kwa sasa halmashauri pekee zinadai takribani Shilingi Milioni 50 huku wanunuzi wakidai takribani Shilingi Milioni 100, hali ambayo alionya kuwa inaweza kuhatarisha uhakika wa soko la mazao na bidhaa mbalimbali mkoani humo ikiwa hatua hazitachukuliwa.

Kwa upande wake, Mrajisi Msaidizi wa Vyama vya Ushirika mkoani Geita, Bi. Doreen Mwanry, amewahimiza wananchi ambao bado si wanachama kujiunga na ushirika ili kupata huduma sahihi. 

Alieleza kuwa mkoa una jumla ya vyama 629 vyenye wanachama 5,084, na tayari vyama hai 304 vimeshasajiliwa kwenye Mfumo wa kusajili na kusimamia vyama vya ushirika nchini (MUVU).

Naye Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa, Dkt. Elfas Msenya, ametoa wito kwa AMCOS kusimamia taratibu za mfumo wa stakabadhi ya ghala kutokana na mafanikio makubwa yaliyopatikana kwenye zao la dengu msimu uliopita. 

Alisisitiza kuwa kufuata taratibu hizo kutawezesha mazao yote kuingizwa kwenye mfumo na kuhakikisha wakulima wanapata faida kulingana na bei elekezi zilizotangazwa. 









Mwenyekiti wa Chama cha Wanawake Wachimbaji Madini Tanzania (TAWOMA) Mkoa wa Dodoma, Jesca Nsamba, amesema wanawake wanaendelea kunufaika na mageuzi yanayofanyika katika sekta ya madini, huku akitoa pongezi kwa serikali kwa mchango wake mkubwa katika kukuza sekta hiyo.

Ameyasema hayo leo jijini Dodoma wakati wa kongamano la fursa na mageuzi kwa wanawake katika sekta ya madini, ambapo amebainisha kuwa wanawake wamekuwa miongoni mwa wanufaika wakubwa wa juhudi hizo.

Ameeleza kuwa licha ya msaada unaotolewa na serikali, wanawake wamekuwa wakionyesha juhudi binafsi kwa kuhakikisha wanatekeleza majukumu yao kwa bidii bila kusubiri kufanyiwa kila kitu na  kupitia TAWOMA, wameendelea kuweka mikakati ya kuwainua wanawake ili waweze kunufaika kikamilifu na fursa zilizopo katika sekta ya madini nchini.

Nsamba amesisitiza kuwa si muda mrefu tangu wanawake waanze kushiriki katika shughuli za madini, ambazo hapo awali zilionekana kuwa ni kazi za wanaume pekee, hata hivyo kwa sasa mafanikio yao yanaonekana wazi, huku wanawake wengi wakijitokeza na kushiriki kikamilifu katika shughuli hizo na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.

Amezitaja changamoto zinazowakabili wanawake katika sekta hiyo kuwa ni pamoja na ukosefu wa mitaji na vifaa, akitoa wito kwa wadau na wafadhili kuongeza msaada zaidi ili kuwawezesha kufikia malengo yao, pia amewahimiza wanawake kuwa na ujasiri na kujiamini, akieleza kuwa wana uwezo mkubwa wa kufanikiwa katika sekta ya madini.




Na Pamela Mollel,Arusha 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, Riziki Shemdoe amesema taasisi ya mpango wa usalama barabarani (TARSI) ina mchango mkubwa katika kuimarisha taaluma ya uhandisi na kupunguza ajali za barabarani kupitia utoaji wa mafunzo kwa wataalamu nchini.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya siku tatu kwa wahandisi kuhusu usalama barabarani, Shemdoe alisisitiza kuwa serikali inaona umuhimu wa wahandisi kuendelea kupata mafunzo ya mara kwa mara ili kuongeza ufanisi katika ubunifu na usimamizi wa miundombinu salama.

Alieleza kuwa juhudi hizo ni sehemu ya mkakati mpana wa serikali wa kuhakikisha barabara zinakuwa salama zaidi kwa watumiaji wote, ikiwa ni pamoja na madereva, waendesha pikipiki na watembea kwa miguu.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TARSI, Maliki Barongo, alisema taasisi hiyo imejikita katika kutoa elimu na tafiti zinazolenga kupunguza ajali za barabarani, huku akihimiza wadau kushirikiana kwa karibu ili kufikia malengo hayo.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Utafiti kutoka Taasisi ya Mifupa (MOI), Dkt. Joel Bwemelo, alieleza umuhimu wa kuchukua tahadhari na kuzingatia kanuni za usalama barabarani ili kupunguza athari za ajali zinazoweza kuepukika.

Aidha, Laurent Maganga kutoka Norplan Tanzania alipendekeza elimu ya usalama barabarani iingizwe katika mitaala ya uhandisi, akisema hatua hiyo itasaidia kuzalisha wahandisi wenye uelewa mpana wa masuala ya usalama tangu wakiwa vyuoni.

Mafunzo hayo yamewakutanisha wahandisi kutoka maeneo mbalimbali nchini, yakilenga kubadilishana uzoefu na mbinu bora za kitaalamu zitakazochangia kuboresha ubora wa barabara pamoja na kupunguza ajali zinazotokana na mapungufu ya miundombinu.







Farida Mangube, Morogoro 

RASI wa Ndaki ya Kilimo katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA, Dkt. Nyambilila Amuri amesema chuo hicho kinaendelea kuimarisha matumizi ya teknolojia ya ndege nyuki (Drones) katika kufundishia kilimo cha kisasa.

Anasema matumizi ya drones yanafanyika kwa kushirikiana na kampuni ya Agrimazao, huku akibainisha kuwa teknolojia hiyo imeanza kutumika tangu mwaka jana na inalenga kuongeza uzalishaji, tija pamoja na ufanisi wa matumizi ya pembejeo za kilimo.

Dkt Nyambilila amesema hayo wakati wa mafunzo kivitendo kwa wanachuo wanaosomea shahada za Kilimo katika chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo,SUA.

Kwa upande wake Makamu Mkuu wa chuo Kikuu cha Sokoine Profesa Rafael Chibunda anasema hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa kuboresha mitaala na kuwaandaa wahitimu wenye ujuzi unaokidhi mahitaji ya soko la ajira, huku akieleza kuwa chuo hicho tayari kimenunua ndege nyuki tatu na kinatarajia kuongeza zaidi.

Makamu mkuu huyo wa Chuo kikuu cha Sokoine akasema wameongeza pia Teknolojia  ya matrekta chuoni hapo ili kurahisisha kufundishia na wanafunzi kujifunza zaidi Kilimo cha Kisasa na matengenezo ya mitambo ya Kilimo ili kuzalisha wataalamu wengi zaidi.

Wakizungumzia teknolojia hiyo, baadhi ya wanachuo wanasema imewarahisishia ujifunzaji kwa vitendo na kupunguza changamoto za kilimo cha kizamani.

Elizabeth Salim, mwanafunzi wa Shahada ya Uzalishaji wa Mazao na Usimamizi anasema drones zinasaidia kufanya kilimo kuwa rahisi na rafiki kwa mazingira pamoja na kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi.

Kwa upande wake, Frank Luhanuza anayesomea Uchumi wa Kilimo na Kilimo Biashara anasema matumizi ya teknolojia hiyo yanatoa fursa kwa vijana kujiajiri na kupunguza gharama za uzalishaji, hivyo kufanya kilimo kuwa sekta yenye mvuto zaidi kwa kizazi cha sasa.










Na Karama Kenyunko Michuzi Tv 


JUMLA ya vijana na watoto 75,500 wanatarajiwa kufanyiwa uchunguzi wa ugonjwa wa Selimundu katika mradi wa miaka mitatu unaotekelezwa nchini Tanzania na Kenya, hatua inayolenga kubaini mapema wenye tatizo hilo na kuwapatia huduma stahiki.

Katika mpango huo, watoto wachanga 45,000 watafikiwa, huku watoto wa chini ya miaka mitano wakiwa 12,500 na vijana 18,000 wakipangwa kunufaika na uchunguzi huo.

Akizungumza kwa niaba ya Mganga Mkuu wa Serikali wakati wa uzinduzi wa mradi huo, Dkt. Gunini Kamba amesema bado kuna changamoto ya kuwabaini mapema watoto na vijana wenye selimundu hali inayochangia kuchelewa kwa huduma muhimu. Ameeleza kuwa utekelezaji wa mradi huo utasaidia kuongeza ufanisi wa utambuzi wa mapema na matibabu.

Takwimu zinaonesha kuwa kati ya asilimia 15 hadi 20 ya Watanzania wana vinasaba vya selimundu huku ugonjwa huo ukichangia vifo vya asilimia 5 hadi 7 kwa watoto walio chini ya miaka mitano.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Wataalam Wanaopambana na Selimindu nchini Tanzania, Dkt. Elisha Osati, amesema mradi huo pia utalenga kuwafikia vijana ili wafahamu hali zao za vinasaba, akisisitiza kuwa hali hiyo haiwezi kujulikana bila kupimwa.

Amefafanua kuwa mtu hupata ugonjwa wa sikoseli pale anaporithi vinasaba viwili kutoka kwa wazazi wote wawili, hivyo elimu kwa vijana ni muhimu ili waweze kufanya maamuzi sahihi wanapoingia kwenye mahusiano.

Naye shujaa wa Selimundu, Samwel Maingu, amesema aligundulika kuwa na ugonjwa huo akiwa na umri wa miaka 18, akihimiza jamii kujenga utamaduni wa kupima mapema ili kupunguza maambukizi mapya ya ugonjwa huo.
Dkt. Gunini Kamba, akizungumza na wadau wa ugonjwa wa Selimundu kwa niaba ya Mganga Mkuu wa Serikali wakati wa uzinduzi wa mradi wa miaka mitatu wa Selimundu unaotekelezwa Tanzania na Kenya. Uzunduzi huo umefanyika leo Aprili 23, 2026 jijini Dar es Salaam
Shujaa wa Selimundu, Samwel Maingu akizungumza  wakati wa uzinduzi wa mradi wa miaka mitatu wa Selimundu unaotekelezwa Tanzania na Kenya. Uzinduzi huo umefanyika leo Aprili 23, 2026 jijini Dar es Salaam.




 

Na Janeth Raphael MichuziTv 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema matukio ya vurugu yaliyotokea wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025 yalikuwa ya kushtua na kutikisa ustawi wa taifa, akibainisha kuwa uchunguzi rasmi umebaini kuwa yalipangwa kwa makusudi, yaliratibiwa na pia kufadhiliwa ili kuvuruga mchakato mzima wa uchaguzi na kudhoofisha amani ya nchi.

Rais Samia ameyasema hayo leo Ikulu jijini Dar es Salaam wakati alipokabidhiwa rasmi ripoti ya Tume ya Uchunguzi wa Matukio ya Uvunjifu wa Amani yaliyotokea katika kipindi cha uchaguzi huo.

Amesema ni muhimu kwa Watanzania kukubali na kuzungumza ukweli kuhusu kilichotokea, akisisitiza kuwa matukio hayo ni funzo kubwa linalopaswa kutumika kuimarisha mustakabali wa taifa na kulinda amani ya kudumu.

“Tusijidanganye, yaliyotokea wakati ule yalitikisa taifa letu. Kwa kweli yalikuwa changamoto kubwa na tumepata somo muhimu,” alisema Rais Samia.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo ya tume, imebainika kuwa baadhi ya watu waliohusika katika vurugu hizo walikuwa wamepata mafunzo maalum, na walitumia vifaa vya uhalifu vilivyolenga kuharibu miundombinu muhimu ya nchi pamoja na kusababisha hofu na taharuki kwa wananchi.

Aidha, ripoti hiyo inaeleza kuwa lengo kuu la matukio hayo lilikuwa kuvuruga mchakato wa uchaguzi, kushambulia miundombinu ya msingi ya taifa, pamoja na kuathiri utoaji wa huduma za kijamii ili hatimaye kudhoofisha uchumi na utendaji wa Serikali.

“Vurugu zilianza siku ya uchaguzi, zikilenga mfumo mzima wa nchi,” aliongeza Rais Samia.

Katika hotuba yake, Rais Samia pia amevipongeza vyombo vya ulinzi na usalama kwa jitihada zao za haraka na za ufanisi zilizosaidia kurejesha hali ya utulivu wakati wa na baada ya matukio hayo, hatua iliyosaidia kuzuia madhara makubwa zaidi kwa wananchi na taifa kwa ujumla.

Amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kuchukua hatua stahiki kwa mujibu wa sheria ili kuhakikisha kuwa amani, utulivu na demokrasia ya nchi vinalindwa kwa nguvu zote.





Na Janeth Raphael-MichuziTv

Tume ya Uchunguzi: Ghasia za Uchaguzi Mkuu 2025 Zilipangwa, Zikafadhiliwa na Kuratibiwa na Watu Wenye Mafunzo

Tume ya kuchunguza matukio ya uvunjifu wa amani yaliyotokea wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, imebaini kuwa ghasia hizo zilikuwa zimepangwa kwa makusudi, kuratibiwa kwa umakini na kufadhiliwa na watu waliopata mafunzo maalum.

Akitoa taarifa ya Tume hiyo kwa Rais wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo Alhamisi Aprili 23, 2026, Mwenyekiti wa Tume hiyo ambaye ni Jaji Mkuu Mstaafu, Mohamed Othman Chande, amesema uchunguzi umebaini kuwepo kwa mtandao ulioratibu matukio hayo katika maeneo mbalimbali nchini.

Kwa mujibu wa Tume, wahusika walitumia mbinu mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuwashawishi vijana na watu waliokuwa katika mazingira magumu ya maisha, ikiwemo wasio na ajira na waliokata tamaa, ili kuwashirikisha katika maandamano na ghasia hizo.

Aidha, imeelezwa kuwa baadhi ya vijana walitumiwa kupitia maeneo ya vyuo, masoko na maeneo yenye mikusanyiko mikubwa ya watu, ambapo walikuwa wakishawishiwa na kuandikishwa kushiriki katika vurugu hizo.

Tume hiyo imesema watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi, waendesha pikipiki pamoja na wajasiriamali wadogo walieleza kupewa fedha kati ya Shilingi 10,000 hadi 50,000 kama motisha ya kushiriki, huku wakiahidiwa ajira na maisha bora.

Kwa mujibu wa ushahidi uliokusanywa, kati ya tarehe 12 Oktoba hadi 28 Oktoba 2025, washiriki wengi waliwekwa pamoja, wakapewa mafunzo na kuandaliwa kwa ajili ya kuanzisha na kushiriki ghasia zilizotokea siku ya uchaguzi.

Jaji Chande ameongeza kuwa uchunguzi umebaini kuwa waliokuwa wakishawishiwa na kuandaliwa ndiyo walioonekana kushiriki kwa wingi katika vurugu hizo, huku waratibu wakuu wakibaki nyuma na kuepuka maeneo ya tukio.

Hali hiyo, kwa mujibu wa Tume, ilisababisha changamoto katika kuwabaini na kuwakamata wahusika wakuu, ambapo mara nyingi walikamatwa zaidi wananchi wa kawaida waliokuwa wafuata mkumbo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Ripoti ya Tume ya Rais ya Kuchunguza Matukio ya Uvunjifu wa Amani wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 2025, kutoka kwa Mwenyekiti wa Tume hiyo, Jaji Mkuu Mstaafu Mhe. Mohamed Chande Othman, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 23 Aprili, 2026.





-Wakaguzi wakuu wa migodi watakiwa kupewa fursa zaidi kuimarisha usalama na utunzaji wa mazingira


📍KAHAMA

Serikali imeendelea kusisitiza umuhimu wa kuwawezesha Wakaguzi Wakuu wa Migodi pamoja na wachimbaji wadogo nchini ili kuimarisha usalama kazini, kulinda mazingira na kuongeza mchango wa sekta ya madini katika ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Wito huo umetolewa leo Aprili 23, 2026 wilayani Kahama, mkoani Shinyanga na Mkurugenzi wa Huduma za Leseni wa Tume ya Madini, Mhandisi Aziza Swedi, alipokuwa akifungua mafunzo kwa mameneja na Wakaguzi Wakuu wa Migodi ya uchimbaji mdogo kwa niaba ya Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhani Lwamo.

Mafunzo hayo yanawakutanisha washiriki kutoka mikoa ya kimadini ya Kahama, Mbogwe na Shinyanga yakilenga kuimarisha uelewa wa kitaalam, usimamizi bora wa migodi, uzingatiaji wa sheria na kanuni pamoja na kukuza uchimbaji salama na endelevu.

Akizungumza wakati wa ufunguzi huo, Mhandisi Swedi amesema Wakaguzi Wakuu wa Migodi wanapaswa kupewa ushirikiano na mazingira wezeshi ili waweze kutekeleza majukumu yao kikamilifu, hatua itakayosaidia kuzuia ajali migodini, kulinda afya za wachimbaji na kuhifadhi mazingira yanayozunguka maeneo ya uchimbaji.

Amesema mafanikio ya jitihada za Serikali katika kuwawezesha wachimbaji wadogo yanategemea ushirikiano wa wadau wote, hususan mameneja na wakaguzi wa migodi ambao ni nguzo muhimu katika kusimamia uzingatiaji wa sheria, kanuni na viwango vya usalama.

“Serikali inalenga kuhakikisha shughuli za uchimbaji zinaendelea kuchangia maendeleo ya Taifa huku zikifanyika kwa njia salama zisizoathiri mazingira, afya za wachimbaji na ustawi wa jamii,” amesema.

Aidha, amesema kupitia usimamizi madhubuti, nchi inaweza kufikia azma ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuongeza mchango wa sekta ya madini katika Pato la Taifa kutoka asilimia 10 ya sasa hadi asilimia 12.5 ifikapo mwaka 2030.

Ameeleza kuwa wachimbaji wadogo tayari wanachangia takribani asilimia 40 ya mapato yatokanayo na shughuli za madini, hali inayoonesha umuhimu wao katika uchumi wa Taifa, huku akiwataka wamiliki wa migodi kuhakikisha taarifa za uzalishaji na kumbukumbu muhimu zinatunzwa ipasavyo ili Serikali ipate mapato stahiki kwa wakati.

Mhandisi Swedi pia ameonya kuhusu athari za uchimbaji usiozingatia taratibu, akitaja matumizi holela ya kemikali hatarishi kama zebaki na sayanaidi pamoja na vumbi la silica kuwa chanzo cha magonjwa hatari ikiwemo silicosis, kifua kikuu na saratani.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Migodi na Mazingira kutoka Tume ya Madini, Mhandisi Hamisi Kamando, amesema Wakaguzi Wakuu wa Migodi wanapaswa kuwasilisha taarifa za ukaguzi mara kwa mara ili kuiwezesha Serikali kubaini mapema vihatarishi vinavyoweza kusababisha ajali na kuchukua hatua za kinga kwa wakati.

Amesema bado kuna changamoto katika baadhi ya maeneo ya migodi ikiwemo ukiukwaji wa sheria, ukosefu wa kumbukumbu sahihi za uzalishaji, ukwepaji wa kodi na utoroshaji wa madini, hivyo mafunzo hayo yanalenga kuwajengea washiriki uwezo wa kuwa mabalozi wa uzingatiaji wa sheria na taratibu za sekta hiyo.

“Tunataka kuona wachimbaji wanaingia migodini salama na kurejea majumbani mwao salama kila siku. Uhai wa binadamu una thamani kubwa kuliko madini,” amesema Mhandisi Kamando.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji Wadogo wa Madini Mkoa wa Shinyanga (SHIREMA), Hamza Tandiko, amesisitiza umuhimu wa weledi kwa wachimbaji na utoaji wa taarifa sahihi za shughuli za uchimbaji, huku akipongeza mchango wa wakaguzi katika kupunguza ajali na madhara migodini.













Top News