Dar es Salaam, Julai 10, 2026

Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) umewahimiza wananchi waliojiajiri nchini kujiunga na kuchangia katika Mfuko huo ili kujijengea akiba, kupata kinga ya kijamii na kuwa na uhakika wa maisha ya sasa na baadaye.

Wito huo umetolewa na Mkurugenzi wa Usimamizi wa Rasilimali Watu na Utawala, Bw. Ekwabi Mujungu, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Bw. Masha Mshomba, wakati akifungua Siku Maalumu ya Hifadhi ya Jamii kwa Wananchi Waliojiajiri iliyofanyika Julai 10, 2026 katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba).

Akizungumza wakati wa ufunguzi huo, Bw. Mujungu alisema Siku Maalumu ya Hifadhi ya Jamii kwa Wananchi Waliojiajiri ni sehemu ya mkakati wa NSSF wa kusogeza huduma karibu na wananchi na kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa hifadhi ya jamii kwa wananchi waliojiajiri, ambao ni sehemu muhimu ya ukuaji wa uchumi wa nchi.

"Wananchi wengi wanaojiajiri hupata kipato kupitia shughuli wanazozifanya, lakini bila kuwa na utamaduni wa kujiwekea akiba wanaweza kujikuta wakikabiliwa na changamoto wanapofikia uzee au wanapopoteza uwezo wa kufanya kazi. Kujiunga na NSSF ni hatua muhimu ya kujenga uhakika wa maisha ya sasa na ya baadaye," alisema Bw. Mujungu.

Alisema Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kuweka mazingira wezeshi ya kupanua wigo wa hifadhi ya jamii ili wananchi wote, bila kujali aina ya shughuli wanazofanya, wanufaike na huduma za mifuko ya hifadhi ya jamii.

"Tunawahimiza wananchi wote waliojiajiri kutumia fursa hii kujiunga na kuchangia NSSF. Mtu anapoanza kuweka akiba mapema, anajijengea msingi imara wa kunufaika na mafao mbalimbali yatakayomsaidia yeye na familia yake pale yatakapohitajika," alisisitiza.

Kwa upande wake, Meneja wa NSSF Mkoa wa Kigamboni, Bw. Siraji Kisaka, alisema siku hiyo maalumu imeandaliwa mahsusi kuwafikia wananchi waliojiajiri kwa kuwapatia elimu kuhusu umuhimu wa kujiunga na kuchangia NSSF pamoja na kuwafahamisha mafao na huduma mbalimbali zinazotolewa na Mfuko.

"Lengo letu ni kuhakikisha wananchi waliojiajiri wanapata uelewa sahihi kuhusu hifadhi ya jamii na umuhimu wa kujiunga na kuchangia NSSF. Tunataka wajenge utamaduni wa kujiwekea akiba ili wawe na usalama wa maisha yao ya sasa na ya baadaye," alisema Bw. Kisaka.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Uwezeshaji Wanawake Tanzania (TAWEN), Florence Massunga, aliwataka wananchi waliojiajiri kuitumia fursa hiyo kujiunga na NSSF, akisema kufanya hivyo kutawasaidia kujenga usalama wa kifedha na kupunguza utegemezi wanapokumbwa na changamoto za maisha.

Baada ya ufunguzi wa shughuli hiyo, wananchi waliojiajiri walipewa elimu kuhusu mfumo wa hifadhi ya jamii, utaratibu wa kujiunga na kuchangia NSSF, mafao mbalimbali yanayotolewa na Mfuko pamoja na umuhimu wa kujenga utamaduni wa kujiwekea akiba mapema ili kuwa na uhakika wa maisha ya sasa na baadaye.

Siku Maalumu ya Hifadhi ya Jamii kwa Wananchi Waliojiajiri ni sehemu ya shughuli za NSSF katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam, zenye lengo la kusogeza huduma karibu na wananchi, kuongeza uelewa kuhusu hifadhi ya jamii na kuwahamasisha wananchi waliojiajiri kujiunga na kuchangia NSSF.





















Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Idara ya Mambo ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa, Ndg. Rabia Abdalla Hamid, leo Julai 20, 2026 akiwa mkoani Mbeya amekutana na kusikiliza changamoto, maoni na mapendekezo kutoka kwa makundi mbalimbali ya kijamii.

Makundi yaliyowasilisha hoja zao ni pamoja na wakulima, wafugaji, wachimba madini, wafanyabiashara, wavuvi, mama na baba lishe, machinga, waendesha usafirishaji, mafundi ujenzi, mafundi gereji, wanamichezo, walimu wazalendo, wazee wastaafu pamoja na vikundi mbalimbali vya kijamii.

Ndg. Rabia alipokea kero, ushauri na mapendekezo yaliyowasilishwa na wananchi hao, huku baadhi ya hoja zikijibiwa na nyingine kutolewa maelekezo kwa ajili ya ufuatiliaji zaidi.

Baada ya kikao hicho, Ndg. Rabia aliwataka wananchi kuendelea kulinda amani ya Tanzania, akisisitiza kuwa amani ni msingi wa maendeleo endelevu na kila Mtanzania ana wajibu wa kuhakikisha nchi inaendelea kuwa salama na yenye utulivu ili wananchi waendelee kufanya shughuli za uzalishaji kwa maendeleo ya taifa.








Waziri wa maliasili na utalii Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) leo tarehe 10 julai, 2026 amekutana na bodi ya wakurugenzi mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro katika ofisi za mamlaka hiyo zilizopo Karatu mkoani Arusha na kusisitiza umuhimu wa bodi hiyo kufuatilia kwa karibu shughuli zote za utendaji ili kuanza mwaka mpya wa fedha 2026/2027 kwa kasi na ufanisi.

Mhe. Kijaji amesema kuwa bajeti ya mwaka mpya wa fedha inaanza na utekelezaji wa dira ya taifa ya maendeleo ya mwaka 2050 hivyo vikao vyake na bodi za taasisi zilizopo chini ya wizara vina lengo la kuanza utekelezaji wa dira, bajeti na ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa pamoja.

Ameitaka bodi hiyo kuongeza nguvu katika kuimarisha uhifadhi, kutangaza utalii na kusimamia maendeleo ya jamii na kusisitiza kuwa jitihada hizo ziendane na kasi ya kukamilisha miundombinu wezeshi ikiwemo barabara kuu ya Loduare hadi Golini, kuimarisha mawasiliano ndani ya eneo lote la hifadhi, kukamilisha mradi wa fensi ya umeme ili kupunguza migongano kati ya wanyamapori na wananchi, kudhibiti ujangili na kuendelea kuimarisha mahusiano ya hifadhi na wananchi wanaoizunguka.

“Tulinde uhifadhi wa Ikolojia ya Ngorongoro kwa wivu mkubwa, tuendelee kubuni mazao mapya ya utalii na kuyatangaza, tujipange kikamilifu kuhakikisha Ngorongoro kama premium destination inawafikia na kuwashawishi wageni watakaohudhuria matukio ya AFCON, mkutano wa umoja wa Mabunge duniani, tuzo za dunia za utalii na shindano la Miss world ambapo matukio yote yatafanyika Tanzania kati ya mwezi oktoba 2026 na Julai mwaka 2027” amesisitiza Dkt. Kijaji.

Katibu wa Bodi, ambae ni kamishna wa Uhifadhi Ngorongoro Abdul-Razaq Badru amemueleza Mhe. waziri kuwa, Ngorongoro imepiga hatua ya kimageuzi kwenye mifumo ya kidijitali (ICT Transformation), uhifadhi endelevu kwa kuimarisha doria za kisasa, kuboresha miundombinu hasa barabara ya tabaka gumu kutoka geti la loduare hadi Seneto (km 29.5) kwa gharama ya TZS 80.3 bilioni

Badru ameongeza kuwa katika mwaka wa fedha 2025/26 eneo la Ngorongoro idadi ya watalii ilifikia 1,061,620 na fedha shilingi 269.5 Bilioni zilikusanywa. Ngorongoro imeendelea na jitihada za kulinda hadhi tatu za kimataifa kutoka UNESCO ambazo ni Urithi wa Dunia (World Heritage Site), Hifadhi ya Biosphere (Man and Biosphere Reserve), na Geopark ya Dunia (Ngorongoro-Lengai Global Geopark) ili ziendelee kuinufaisha nchi yetu.

Kwa upande wake makamu mwenyekiti wa Bodi ya wakurugenzi Ngorongoro Dkt. Harriet Mtae amemueleza Mhe waziri kuwa, katika kipindi cha miezi sita (06) iliyopita bodi ya Ngorongoro imetekeleza majukumu kwa kuzingatia sheria, kanuni pamoja na maelekezo ya Serikali ili kuhakikisha Mamlaka inatekeleza kikamilifu dhamana yake ya kuhifadhi maliasili za Wanyamapori, malikale na urithi wa dunia, kuendeleza utalii endelevu na kuboresha shughuli za maendeleo ya jamii.



Na Janeth Raphael MichuziTv

Vigogo wanane wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT) wameendelea kushikiliwa rumande baada ya upande wa Jamhuri kueleza kuwa upelelezi wa kesi ya uhujumu uchumi na rushwa inayowakabili bado haujakamilika.

Shauri hilo lilipotajwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Dodoma jana, Julai 9, 2026, Wakili wa Serikali, Gothard Mwingira, aliiambia mahakama kuwa upelelezi umefikia hatua za mwisho, lakini bado haujakamilika. Alieleza kuwa upande wa mashtaka unasubiri kibali cha Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) kabla ya kuendelea na hatua zinazofuata za shauri hilo.

Kutokana na maelezo hayo, upande wa Jamhuri uliomba mahakama ipange tarehe nyingine kwa ajili ya kutajwa kwa kesi hiyo wakati taratibu za upelelezi zikikamilishwa.

Washtakiwa katika shauri hilo ni aliyekuwa Rais wa CWT, Leah Ulaya, Rais wa sasa wa CWT, Suleiman Ikomba, aliyekuwa Katibu Mkuu wa chama hicho, Maganga Japhet, Katibu Mkuu wa sasa, Joseph Misalaba, pamoja na Nashon Kidudu, Baraka Mbonalibha, Wambura Kihengu na Angelina Wambura. Pia kampuni ya Pyrite and Industries Company Limited inatajwa kama mshtakiwa katika kesi hiyo.

Viongozi hao walifikishwa kwa mara ya kwanza mahakamani Mei 25, 2026, ambapo walisomewa jumla ya mashtaka 14 yanayohusisha uhujumu uchumi na rushwa.

Hata hivyo, hawakutakiwa kujibu mashtaka hayo kwa kuwa Mahakama ya Hakimu Mkazi haina mamlaka ya kusikiliza kesi zinazohusu uhujumu uchumi.

Shauri hilo litaendelea kutajwa mahakamani baada ya upande wa Jamhuri kukamilisha upelelezi na kupata kibali kinachohitajika kutoka kwa Mkurugenzi wa Mashtaka.





New York, Marekani


Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeeleza hatua zake za kuanza kutekeleza Mpango wa Nne wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano, 2026/27–2030/31 (FYDP IV), ambao ni mpango wa kwanza wa muda wa kati wa kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Hayo yamelezwa na Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais–Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt. Tausi Mbaga Kida, wakati wa mkutano wa pembezoni mwa Jukwaa la Ngazi ya Juu la Siasa la Umoja wa Mataifa linalosimamia Utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (HLPF 2026), uliofanyika katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, New York, Marekani.

Mkutano huo, wenye mada “Driving Industrial and Inclusive Economic Transformation: Financing, Innovation and Sustainable Growth in Agricultural and Blue Economy Value Chains”, uliandaliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Maendeleo ya Mitaji (UNCDF), pamoja na UNDP, UNIDO na washirika wengine.

Dkt. Kida alisema Tanzania inaingia katika awamu mpya ya utekelezaji wa maendeleo inayolenga kubadilisha mafanikio ya ukuaji wa uchumi na uwekezaji katika miundombinu kuwa ongezeko la uzalishaji, ajira zenye tija, mauzo ya nje, ongezeko la thamani ya bidhaa na ustawi mpana wa wananchi.

Dkt. Kida alisema uchumi wa Tanzania kwa sasa unakua kwa asilimia 5.9 na unatarajiwa kufikia asilimia 6.3 ifikapo mwisho wa mwaka huu. Ukuaji huo ulichangiwa na kuimarika kwa shughuli mbalimbali za uzalishaji na huduma, pamoja na kuendelea kwa uwekezaji katika miundombinu na miradi ya kimkakati.

Hata hivyo, alisisitiza kuwa lengo si kasi ya ukuaji pekee, bali ukuaji unaogusa maisha ya wananchi wote. “Lengo letu si kuongeza ukubwa wa uchumi pekee. Tunataka ukuaji unaoongeza kipato cha wananchi, unaotengeneza ajira, unaopunguza umaskini na unaowezesha wanawake, vijana, wakulima wadogo na wajasiriamali kushiriki kikamilifu katika uchumi,” alisema Dkt. Kida.

Dkt. Kida alibainisha kuwa kilimo, misitu na uvuvi vinaendelea kuwa sehemu muhimu ya uchumi wa Tanzania, vikichangia asilimia 24.3 ya Pato la Taifa mwaka 2025. Alisema mchango wa uvuvi katika Pato la Taifa uliongezeka kutoka asilimia 1.9 mwaka 2020 hadi asilimia 2.2 mwaka 2025, hatua inayoonesha fursa zinazoongezeka katika uchumi wa buluu.

“Tunataka kuondoka katika uchumi unaouza malighafi na kuelekea uchumi unaosindika, unaoongeza thamani, unaotumia teknolojia na unaounganisha wazalishaji wa ndani na masoko ya kitaifa, kikanda na kimataifa,” alisema.

Dkt. Kida pia alisema Tanzania itawasilisha Mapitio ya Tatu ya Hiari ya Nchi ya utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu tarehe 14 Julai 2026.

Mapitio hayo yanaonesha maendeleo yaliyopatikana katika maji safi, nishati, miundombinu, afya, usafiri, teknolojia ya kidijitali na uimarishaji wa rasilimali za ndani.

Kwa upande wake, Balozi na Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, New York, Mhe. Togolani Edriss Mavura, alisema mageuzi ya viwanda barani Afrika yanapaswa kuwa jumuishi na kuwanufaisha wakulima wadogo, wanawake, vijana, wavuvi, wafugaji, biashara ndogo na washiriki wa sekta isiyo rasmi.

Alisisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kimataifa katika teknolojia, uwekezaji, masoko, ujuzi, fedha za maendeleo na ujenzi wa minyororo ya thamani inayounganisha nchi za Afrika.

Ofisa Mkuu wa Fedha wa UNCDF, Bw. Karen Vardanyan, aliitaja Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zinazoonesha namna fedha bunifu zinavyoweza kutumika kuharakisha maendeleo katika ngazi ya taifa na mamlaka za serikali za mitaa.

Alieleza kuwa upatikanaji wa nishati safi ya kupikia umeongezeka kutoka asilimia 6.9 mwaka 2021 hadi asilimia 28.6 mwaka 2025. Maendeleo hayo yanaungwa mkono na utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia, uwekezaji wa sekta binafsi na juhudi za Serikali za kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa.

Bw. Vardanyan pia alitaja Tanga UWASA Green Revenue Bond, iliyokusanya dola za Marekani milioni 20.8 kwa ajili ya miundombinu ya maji inayohimili mabadiliko ya tabianchi. Hatifungani hiyo ilikuwa ya kwanza ya kijani katika ngazi ya mamlaka ya chini ya kitaifa Afrika Mashariki, huku wawekezaji wa ndani wakichangia asilimia 65 ya uwekezaji wote.

Mifano mingine iliyotajwa ni PesaTech Accelerator, inayosaidia ubunifu wa huduma za kifedha na biashara zinazoongozwa na vijana, pamoja na mfumo wa LoCAL unaowezesha mamlaka za serikali za mitaa kuongeza uwekezaji unaohimili athari za mabadiliko ya tabianchi.

Bw. Vardanyan alitoa wito kwa Serikali, taasisi za fedha, sekta binafsi na washirika wa maendeleo kubadili ahadi za kimataifa kuwa miradi inayoweza kufadhiliwa na uwekezaji halisi katika kilimo, uchumi wa buluu, viwanda, maji, nishati na miundombinu.

Mkutano huo ulihitimisha kuwa utekelezaji wa Dira 2050 na FYDP IV utahitaji ushirikiano madhubuti kati ya Serikali, sekta binafsi, taasisi za fedha, Umoja wa Mataifa, washirika wa maendeleo, asasi za kiraia na jamii.

Dira 2050 inalenga kuifanya Tanzania kuwa nchi yenye uchumi wa kipato cha kati cha juu, yenye Pato la Taifa la dola za Marekani trilioni moja, pato la wastani kwa mtu linalozidi dola 7,000 na kuondoa umaskini ifikapo mwaka 2050.










Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Hemed Suleiman Abdulla, amesema kitabu cha 'Falsafa ya Sheria ya Mama Samia' kinaakisi mchango mkubwa wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha utawala wa sheria kwa ajili ya kuleta maendeleo. 

Amesema hayo leo wakati akizindua kitabu hicho katika ukumbi wa Maktaba ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, akimwakilisha Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba. Abdulla pia amewataka Watanzania kuendelea kudumisha amani na mshikamano. "Bila amani, maendeleo hayatafanyika. Nawaomba wale wenye mawazo tofauti waungane na Watanzania wengine kuwa wazalendo na kulinda amani ya nchi yetu," amesema.

Akizungumzia maudhui ya kitabu, Abdulla amesema waandishi wake wamekitazama sheria kama mfumo unaogusa uchumi wa jamii nzima na sio kwa upana mdogo. Amesisitiza kuwa kitabu kimegusa maeneo matatu muhimu. La kwanza ni mapato ya ndani ambayo yameongezeka kwa kiasi kikubwa kipindi cha awamu ya sita, na kusaidia serikali kugharamia miradi ya barabara, reli, umeme na afya. 

La pili ni mageuzi ya VAT na kodi nyingine ambapo mapato yameongezeka na kuonesha kodi zinaendana na uchumi wa kidigitali. La tatu ni uwekezaji ambapo maboresho ya Sheria ya Uwekezaji ya 2022 yamerahisisha huduma na kuondoa urasimu. "Serikali ya awamu ya sita inataka uwekezaji unaozalisha ajira, unaoongeza teknolojia na ushiriki wa Watanzania katika uchumi," amesema Abdulla.

Kwa upande wake, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Hamza Johari, amesema kitabu hicho kinaonesha jinsi sheria ilivyo chombo cha kuimarisha uchumi wa taifa na si cha udhibiti tu. "Sheria si maandishi tu bali ni miundombinu ya taifa. Ikiandikwa vibaya inaweza kuchelewesha maendeleo, ikiwa na utata inaleta migogoro, na ikiwa dhaifu inaleta matumizi mabaya ya mamlaka," amesema. 

Johari amemshukuru Rais Samia kwa kuendelea kuongoza nchi kwa mwelekeo wa maridhiano ili mageuzi ya uchumi, usawa na maendeleo yaweze kufikiwa.






Top News