Waziri wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Dennis Londo, ametembelea banda la Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji katika maonesho ya Sabasaba 2026 na kupata maelezo kuhusiana na Majukumu na utendaji kazi wa Ofisi hiyo na kukabidhiwa Mfuko wenye ujumbe wa Dira 2050 Wekeza Tanzania.

Aidha, Naibu Waziri Dennis Londo amepongeza utendaji kazi wa Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji ikiwa ni pamoja na kuhamasisha uwekezaji na kuanza kwa utekelezaji wa Dira 2050 ikiwa ni injini ya kukuza uchumi wa Nchi.

Waziri wa Fedha Balozi Khamis Mussa Omary Akizungumza  katika Banda la Chuo cha  Uhasibu Arusha (IAA) wakati alipotembelea banda hilo katika maonesho ya 50 ya Biashara Kimataifa yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (Sabasaba) jijini Dar es Salaam.

Kamishina wa Sensa ,Spika Mstaafu Anna Makinda akisaini Kitabu katika Banda la Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA)  wakati alipotembelea banda hilo katika maonesho ya 50 ya Biashara Kimataifa yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (Sabasaba) jijini Dar es Salaam.




*Yawahimiza wananchi kutembelea banda

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
BARAZA la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET) limewahimiza wananchi kutembelea banda lake katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) ili kujionea mafanikio makubwa yaliyopatikana katika utekelezaji wa elimu ya amali na mafunzo ya ufundi stadi nchini.

Banda hilo limekuwa kivutio kutokana na uwepo wa wanafunzi kutoka shule za sekondari zenye mkondo wa amali, ambao wanaonesha kwa vitendo ujuzi, ubunifu na maarifa waliopata kupitia masomo yao.

Wanafunzi hao wanawasilisha kazi mbalimbali zinazoonyesha namna elimu hiyo inavyowaandaa kujiajiri, kuajirika na kuendelea na masomo ya juu wakiwa na msingi imara wa taaluma.

Mbali na maonesho ya vitendo, wataalamu wa NACTVET wanatoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu ya Baraza katika kusimamia ubora wa elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi, pamoja na kueleza fursa za masomo zinazopatikana katika vyuo vinavyosimamiwa na Baraza.

Pia wananchi wanapatiwa maelezo kuhusu taratibu za udahili, matumizi ya Namba ya Utambuzi na Tuzo (AVN), upatikanaji wa hati za matokeo na huduma nyingine zinazotolewa na Baraza kwa lengo la kuboresha utoaji wa elimu nchini.

Akizungumza katika maonesho hayo, mwanafunzi wa Kidato cha Tatu katika Shule ya Sekondari Baobab, Careen Maki, alisema mkondo wa amali umemjengea uwezo na kujiamini katika kufikia ndoto yake ya kuwa mhandisi wa umeme.

Alisema kwa sasa anasomea fani ya umeme kupitia mkondo wa amali, jambo ambalo linampa msingi mzuri wa kuendelea na elimu ya juu na kutimiza malengo yake ya kitaaluma.

Kwa upande wake, mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Bwiru mkoani Mwanza, Daud Elias, alisema anasomea fani ya ujenzi kupitia mkondo wa amali na anaamini elimu hiyo itamwezesha kutimiza ndoto yake ya kuwa Mhandisi wa Majengo.

Alieleza kuwa utofauti wa mkondo wa amali ni kwamba unampa mwanafunzi nafasi ya kujifunza kwa vitendo zaidi kuliko nadharia, hali inayoongeza uelewa, kujiamini na uwezo wa kutatua changamoto zinazohusiana na taaluma husika.

NACTVET imesema maonesho ya Sabasaba ni jukwaa muhimu kwa wazazi, wanafunzi, walimu, waajiri na wadau mbalimbali kujifunza kuhusu mchango wa elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi katika kuzalisha wataalamu wenye ujuzi, kukuza ubunifu, kuongeza ajira na kuchochea maendeleo ya uchumi wa Taifa.NACTVET yaonesha mafanikio ya elimu ya amali Sabasaba



Na Mwandishi wetu,

Wakulima wa zao la Korosho  wamemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kuwapatia pembejeo za kilimo licha ya uwepo wa changamoto mbalimbali.

Wakulima hao ambao ni Wakulima wa Korosho wa mkoa wa Mtwara wameendelea kupokea pembejeo za kilimo ikiwemo dawa za maji na dawa ya unga ama Sulphur ambapo hawakusita kupaza sauti zao za pongezi.

"Sisi Wakulima tunatambua jitihada za Rais Samia kutupa pembejeo ambapo hatujaamini kama tungepata kutokana na namna Wakubwa huko Ulaya wanavyopigana vita na hivyo kupelekea uzalishaji kupungua na kupata huku dawa ni Maajabu ambayo Rais Samia ameonyesha namna anavyotupambania sisi Wakulima." alisema Mwananchi ambaye pia ni Mkulima Ndugu Rashid Hamid maarufu kwa jina la Mkapa mkazi wa Nansinji.

Hayo yamejili wakati wa ziara aliyofanya Ndugu Emmanuel Shilatu ambaye ni Afisa Tarafa kujiridhisha juu ya mwenendo wa ugawaji wa pembejeo ambapo zoezi limeendelea vyema.

"Kwa niaba ya Wananchi ningependa kuungana nao kumpongeza Mhe. Rais Samia kwa namna anavyowajali Wakulima kwa kuwapatia pembejeo za kilimo. Anayafanya hayo sanjali na kuwapatia Wataalamu wa kilimo, kuwapatia mbegu na kuwasimamia Wakulima kupata masoko ya mazao Yao kupitia mfumo wa stakabadhi ghalani. Hauwezi kuongelea mafanikio ya Kilimo na Wakulima nchini pasipo kumtaja Rais Samia." Alisema Shilatu 

Halikadhalika Mwenyekiti Kijiji Cha Kivukoni Ndugu Jackson Joseph Milanzi alishukuru kwa pembejeo na kuhaidi kutekeleza maelekezo ya Afisa Tarafa ya kuendelea kusimamia ugawaji wa pembejeo hizo kwa uwazi, haki na usawa kama zoezi linavyoendelea.

Wakulima wa Korosho nchini wameanza kupokea pembejeo za kilimo mapema sana kwa msimu huu tofauti na hapo awali na hivyo wanatarajia kuwa na msimu mzuri wa Korosho kwa mwaka huu na hivyo kupata tija ya uzalishaji.






Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) imesema ushiriki wake katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam Sabasaba unalenga kutoa elimu ya uhifadhi wa wanyamapori, kuhamasisha utalii wa ndani, pamoja na kusogeza huduma kwa wananchi kupitia maonesho ya wanyamapori na uuzaji wa nyara halali za wanyamapori na nyama pori.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam Julai 3, 2026, Mhifadhi Mkuu wa TAWA, Steven Madenge, amesema wananchi wanaotembelea banda la mamlaka hiyo wanapata fursa ya kujionea wanyamapori mbalimbali wakiwemo twiga, simba, chui, fisi, pundamilia, tembo na mamba, hatua inayolenga kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa uhifadhi na kuwavutia kutembelea hifadhi za wanyamapori nchini.

Aidha, amewataarifu wananchi kuwa TAWA imeandaa programu mpya iitwayo Pande Marathon, inayotarajiwa kufanyika Agosti 1, 2026 katika Hifadhi ya Pande, jijini Dar es Salaam, amesema mbio hizo zinalenga kuimarisha afya pamoja na kuendelea kuunganisha wananchi na shughuli za utalii na uhifadhi nchini.









Na Mwandishi Wetu

Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) imesema imejipanga kutumia Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) kutoa elimu kwa wananchi kuhusu haki za binadamu na utawala bora pamoja na huduma mbalimbali zinazotolewa na tume hiyo.

Akizungumza katika banda la Tume hiyo kwenye maonesho hayo, Mkurugenzi wa Sheria wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Ellen Ruyage, alisema wananchi wanaotembelea banda hilo wanapata fursa ya kufahamu majukumu ya tume, kuwasilisha malalamiko yanayohusu ukiukwaji wa haki za binadamu na misingi ya utawala bora, pamoja na kupata ushauri na msaada wa kisheria.

Alisema tume inapokea malalamiko yote yanayohusu uvunjifu wa haki za binadamu na ukiukwaji wa misingi ya utawala bora, kisha kuyafanyia kazi kwa mujibu wa sheria, huku ikitoa maelezo kwa walalamikaji kuhusu hatua zinazochukuliwa.

"Tunapokea malalamiko yote yanayohusiana na uvunjifu wa haki za binadamu na ukiukwaji wa misingi ya utawala bora.

Aidha, tunatoa huduma za msaada wa kisheria pamoja na elimu kuhusu haki za binadamu na utawala bora ili wananchi wajue haki zao na namna ya kuzidai," alisema Ruyage.

Alifafanua kuwa si kila mwananchi anayewasilisha malalamiko yake hukumbana na ukiukwaji wa haki za binadamu au misingi ya utawala bora, bali wakati mwingine tatizo linaweza kuwa nje ya mamlaka ya tume. Hata hivyo, alisema tume huwapa mwongozo wa mahali sahihi pa kupata huduma ili kuhakikisha haki zao hazicheleweshwi.

Ruyage alisema juhudi za tume za kuendelea kutoa elimu zimeongeza uelewa wa wananchi, hali inayowafanya kujitokeza kwa wingi kuripoti matukio ya ukiukwaji wa haki zao na pale wanapoona misingi ya utawala bora haifuatwi.

Aliongeza kuwa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora inaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa ndani na nje ya nchi, ikiwemo mashirika ya kimataifa, hatua ambayo imewezesha huduma zake kuwafikia wananchi wengi zaidi katika maeneo mbalimbali nchini.

Aidha, alitoa wito kwa wananchi kutumia fursa ya maonesho ya Sabasaba kutembelea banda la tume ili kupata elimu, ushauri wa kisheria na kuwasilisha changamoto zozote zinazohusu haki za binadamu na utawala bora.

"Tume yetu iko wazi kwa wananchi wote. Tunawahimiza wajitokeze kupata huduma na elimu ili kujenga jamii inayozingatia haki za binadamu na misingi ya utawala bora," alisisitiza

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Alhaj Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amejumuika na waumini wa dini ya Kiislamu katika Sala ya Ijumaa iliyosaliwa katika Msikiti wa Mubarak Mazrui, uliopo Mombasa, Mkoa wa Mjini Magharibi leo tarehe 03 Julai, 2026.

Akitoa salamu zake kwa waumini baada ya sala hiyo, Rais Dkt. Mwinyi amewanasihi waumini wa dini ya Kiislamu na wananchi kwa ujumla kuendelea kudumisha amani, umoja, upendo na mshikamano, ili Serikali iendelee kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo kwa ajili ya kuimarisha ustawi wa wananchi.

Rais Dkt. Mwinyi amewahakikishia wananchi kuwa nchi ipo salama, hali inayoiwezesha Serikali kutekeleza mipango na miradi yake ya maendeleo kwa mafanikio makubwa, huku akiwahimiza kuendelea kuunga mkono juhudi hizo.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amesisitiza umuhimu wa wananchi kuvumiliana na kusameheana, akieleza kuwa misingi hiyo ni muhimu katika kudumisha amani na utulivu nchini, pamoja na kuwezesha utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo, ikiwemo ujenzi wa miundombinu, uimarishaji wa sekta ya afya, viwanja vya ndege na michezo.

Rais Dkt. Mwinyi ameendelea na utaratibu wake wa kujumuika na waumini wa dini ya Kiislamu katika Sala za Ijumaa kwenye misikiti mbalimbali mijini na vijijini.

















Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
MIXX imewakutanisha wajasiriamali 18 katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba), ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuwawezesha kutangaza bidhaa na huduma zao pamoja na kupanua masoko.

Akizungumza katika maonesho hayo, Mkuu wa Kanda ya Kusini ya Dar es Salaam wa MIXX by YAS, Robert Kasulwa, alisema wajasiriamali hao ni wanufaika wa awamu ya pili ya mradi wa Anzia Ulipo, unaolenga kuwawezesha Watanzania kujikwamua kiuchumi kupitia ujasiriamali.

Kasulwa alisema katika awamu hiyo, jumla ya wajasiriamali 48 wamenufaika na mafunzo pamoja na uwezeshaji wa biashara, huku 18 kati yao wakipata nafasi ya kushiriki maonesho ya Sabasaba ili kutangaza bidhaa zao na kukutana na wateja pamoja na wadau mbalimbali wa biashara.

Alieleza kuwa lengo la mradi huo ni kuwafikia Watanzania wengi zaidi na kuwainua kiuchumi kwa kuwajengea uwezo wa kuanzisha na kukuza biashara endelevu katika maeneo mbalimbali nchini.

"MIXX by YAS inaendelea kushirikiana na wajasiriamali kwa kuwapa fursa za kujifunza, kuonyesha bidhaa zao na kupanua mtandao wa biashara. Tunaamini uwezeshaji huu utachochea ukuaji wa uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla," alisema Kasulwa.

Aliongeza kuwa kampuni hiyo itaendelea kutekeleza programu mbalimbali za uwezeshaji wa wananchi kwa lengo la kuongeza ushiriki wa Watanzania katika shughuli za kiuchumi na kutumia huduma za kifedha za kidijitali kukuza biashara zao.






Na Said Mwishehe,Michuzi TV

MAMLAKA ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya(DCEA) imesema watu 300,000 nchini wanatumia dawa za kulevya aina ya Heroin na kati yao 30,000 wanatumia dawa hizo kwa njia ya kujidunga.

Akizungumza katika semina kwa waandishi wa habari iliyoandaliwa na Mamlaka hiyo kwa ajili ya kuwajengea uelewa, Kamishna wa Kinga na Tiba Dk.Peter Mfisi amesema kwa mujibu wa taarifa ya hali ya dawa za kulevya mwaka 2023 inaonesha watu 300,000 wanatumia Heroin.

“Kati yao watu 30,000 wanatumia dawa za kulevya kwa njia ya kujidunga.Maambukizi ya UKIMWI miongoni mwa wanaojidunga yalikuwa asilimia 36,maambukizi ya homa ya Ini asilimia 60,maambukizi ya kifua kikuu asilimia 11 wakati katika jamii yalikuwa asilimia 0.2.”

Kuhusu madhara ya kiuchumi yanayotokana na matumizi ya dawa za kulevya ,Dk.Mfisi amesema hudhoofisha afya ya mtumiaji hivyo kuathiri uwezo wa kufanya kazi,kutumika kwa rasilimali za taifa katika kuwatibu waraibu na kudhibiti dawahizo

Madhara mengine husababisha mzunguko haramu wa fedha kunakochangia mfumuko wa bei, kuhodhiwa kwa uchumi na wachache, ongezeko la pengo la vipato, kuwepo kwa uwekezaji haramu na utakatishaji fedha.Pia kukithiri kwa rushwa, umasikini kwa familia, jamii na taifa.

Akizungumzia makundi ya dawa za kulevya ameyataja ni Vichangamshi (Stimulants) ambapo huongeza kasi ya utendaji wa mfumo wa fahamu hivyo kuongeza mapigo ya moyo na kasi ya kupumua.Mfano: cocaine na mirungi.

Pia kuna Vipumbaza (Depressants): Hupunguza kasi ya utendaji wa mfumo wa fahamu hivyo kushusha mapigo ya moyo, kasi ya kupumua o Mfano: heroin, valium.

Kundi jingine la dawa za kulevya ni Vileta Njozi (Hallucinogens)ambapo husababisha mtumiaji kuhisi, kuona au kusikia vitu visivyokuwepo au tofauti na uhalisia. Mfano: bangi.

Wakati kundi lingine ni Bangi ambayo hutumika zaidi nchini ikifuatiwa na heroin, mirungi, cocaine na dawa tiba zenye asili ya kulevya.




Na Said Mwishehe,Michuzi TV.

MAMLAKA ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya(DCEA) imetoa mafunzo ya kuwajengea uelewa waandishi wa habari nchini kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu mapambano dhidi biashara haramu ya dawa za kulevya.

Katika mafunzo hayo yaliyofanyika leo Julai 3,2026 jijini Dar es Salaam mada zilizowasilishwa kwa waandishi walioshiriki mafunzo hayo ni Dawa tiba zenye asili ya kulevya,dawa mpya za kulevya& Maabara Bubu pamoja na Madhara ya Dawa za kulevya

Wakati wa mawasilisho hayo ya mada waandishi pia wameelezwa kwa kina kuhusu sheria zinazohusika na udhibiti wa kemikali bashirifu.

Akitoa mada kuhusu kemikali bashirifu na dawa za kulevya Kamishina Msaidizi Uchunguzi kutoka Mamlaka hiyo Ziliwa Machibya amezitaja sheria  hizo ni Sheria ya kemikali za Viwandani na Majumbani (Udhibiti na Usimamizi) Na. 3 ya Mwaka 2003.

Nyingine ni Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Na. 5 yaMwaka 2015 (R.E 2020), Vifungu vya (14, 15, 15A) pamoja na Sheria ya Dawa na Vifaa Tiba Na. 1 ya Mwaka 2003 marekebisho ya Sheria ya Fedha 2019)

Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Kudhibiti Usafirishaji haramu wa Dawa za Kulevya wa mwaka 1988.

Kutokana na sheria hizo pia ametaja kemikamili bashirifu zilizokamatwa maeneo mbalimbali duniani ni Acetone - lita 3360, Ethanol - lita 8750, Azobisisobutyronitrile - kilo 60, Hydrochloric Acid - kilo 1400, Lead acetate - kilo 5000, N-methylformamide-lita 1890.

Dawa nyingine ni Toluene lita 420, Tartaric acid kilo 375, (2-bromoethyl)benzene kilo 13.5, acetic acidi kilo 4.4, Acetone kilo 22.5, benzyl alcohol kilo 434, ethanol kilo 358, hydrochloric acid 1834.36, methylamine 202.5, tartaric acid kilo 21, toluene kilo 67.5

Akitoa mifano ya Uchepushwaji nchini amesema uchunguzi  ulibaini kiasi cha kilo 12 za kemikali bashirifu aina yapseudoephedrine zilikuwa zimechepushwa katika mchakato wa uzalishaji wa dawa za kikohozi na kupelekea uteketezaji wa lita10,000 za dawa zenye pungufu ya kiambata hai cha kemikali hiyo

Pia ukamatwaji wa tani 21.7 za acetic anhydride nchini Pakistani zilizosafirishwa kutoka Tanzania kwa jina bandia la acetic acid

“Mwaka 2025, jumla ya tani 31.76 na lita 183.500 zà kemikali bashirifu zilikamatwa hapa Nchini. Zimezuiliwa kemikali bashirifu tani 734 Kuingia nchini kinyume cha taratibu.

“Kiasi hiki kinahusisha tani 4 za kemikali bashirifu za kutengeneza dawa ya kulevya aina ya fentanaili(kilipangwa kusafirishwa Kwenda Mexico kwa jina bandia la protein biotine) pamoja na kugundulika kwa maabara bubu ya kutengeneza methafetamine mpakani Namanga upande wa Kenya.





Na. Josephine Majura, WF, Nairobi, Kenya.

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), amekutana na kufanya mazungumzo na Uongozi wa Shelter Afrique Development Bank (ShafDB) pembezoni mwa Mkutano Mkuu wa 26 wa Wanahisa wa Taasisi ya Bima ya Biashara na Uwekezaji Afrika (ATIDI), unaoendelea jijini Nairobi, Kenya.

Mazungumzo hayo yalilenga kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Benki hiyo, hususan katika maeneo ya uwekezaji, maendeleo ya makazi na uhamasishaji wa rasilimali za kifedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Pande zote mbili zilikubaliana kuendeleza ushirikiano wa kimkakati utakaongeza fursa za uwekezaji, upatikanaji wa fedha kwa ajili ya miradi ya makazi na miundombinu inayohusiana na sekta hiyo, pamoja na kuchochea maendeleo endelevu ya uchumi.

Kwa upande wake, Serikali ya Tanzania ilieleza utayari wake wa kuendelea kushirikiana na ShafDB katika kubaini na kutumia fursa mbalimbali za maendeleo zitakazochangia kuimarisha upatikanaji wa makazi bora, kukuza sekta ya makazi na kuongeza ustahimilivu wa miundombinu, kwa kuzingatia sheria, taratibu na vipaumbele vya maendeleo vya Taifa.

Naye mwakilishi wa Shelter Afrique Development Bank (ShafDB) Bw. Charles Kazuka, alieleza utayari wa Benki hiyo kuendelea kuimarisha ushirikiano na Serikali ya Tanzania katika kufadhili miradi ya maendeleo ya makazi na miundombinu, akibainisha kuwa Tanzania itaendelea kuwa mshirika muhimu katika utekelezaji wa dhamira ya Benki ya kuchochea maendeleo endelevu barani Afrika.

Shelter Afrique Development Bank (ShafDB) ni taasisi ya kifedha ya kimataifa inayomilikiwa na nchi za Afrika pamoja na taasisi za fedha za maendeleo, ikiwa na dhamira ya kuhamasisha uwekezaji na kutoa ufadhili wa miradi ya makazi na miundombinu inayohusiana na sekta hiyo barani Afrika. Tanzania ni miongoni mwa nchi waanzilishi wa Benki hiyo na imeendelea kushiriki kikamilifu katika shughuli zake tangu ilipoanzishwa, hatua inayoendelea kuimarisha nafasi yake katika kuendeleza ushirikiano wa kikanda kwa manufaa ya maendeleo ya Taifa.

Katika mkutano huo Mhe. Munde, aliambatana na Kaimu Kamishna Idara ya Uendelezaji Sekta ya Fedha, Wizara ya Fedha Bi. Dionisia Mjema na wataalamu kutoka Wizara hiyo.

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), akizungumza na Ujumbe kutoka Shelter Afrique Development Bank (ShafDB), ulioongozwa na Bw. Charles Kazuka, pembezoni mwa Mkutano Mkuu wa 26 wa Wanahisa wa Taasisi ya Bima ya Biashara na Uwekezaji Afrika (ATIDI), unaoendelea jijini Nairobi, Kenya.

Mwakilishi wa Shelter Afrique Development Bank (ShafDB), Bw. Charles Kazuka, akizungumza na Ujumbe kutoka Tanzania uliyoongozwa na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), pembezoni mwa Mkutano Mkuu wa 26 wa Wanahisa wa Taasisi ya Bima ya Biashara na Uwekezaji Afrika (ATIDI), unaoendelea jijini Nairobi, Kenya.

Mazungumza yakiendelea yaliyowahusisha Ujumbe kutoka Tanzania uliyoongozwa na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), na Ujumbe kutoka Shelter Afrique Development Bank (ShafDB) ulioongozwa na Bw. Charles Kazuka, pembezoni mwa Mkutano Mkuu wa 26 wa Wanahisa wa Taasisi ya Bima ya Biashara na Uwekezaji Afrika (ATIDI), unaoendelea jijini Nairobi, Kenya.

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), akifafanua jambo kwa Ujumbe kutoka Shelter Afrique Development Bank (ShafDB) ulioongozwa na Bw. Charles Kazuka, pembezoni mwa Mkutano Mkuu wa 26 wa Wanahisa wa Taasisi ya Bima ya Biashara na Uwekezaji Afrika (ATIDI), unaoendelea jijini Nairobi, Kenya.

Mwakilishi wa Shelter Afrique Development Bank (ShafDB), Bw.Charles Kazuka, akifafanua jambo kwa Ujumbe kutoka Tanzania ulioongozwa na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), pembezoni mwa Mkutano Mkuu wa 26 wa Wanahisa wa Taasisi ya Bima ya Biashara na Uwekezaji Afrika (ATIDI), unaoendelea jijini Nairobi, Kenya.

NA MWANDISHI WETU, DODOMA

Taasisi, mashirika ya umma na kampuni ambazo serikali ina hisa chache zimefanikiwa kuwasilisha gawio kwa serikali lenye thamani ya shilingi trilioni 1.3.

Uwasilishaji huo umefanyika Juni 30, 2026, katika Ikulu ya Dar es Salaam, ambapo Rais Dk. Samia Suluhu Hassan alihudhuria hafla hiyo .

Mbunge wa Viti Maalum wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Mwenyekiti Taifa wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), Mary Chatanda amesema, gawio la shilingi trilioni 1.3, ni udhihirisho wa uimara wa serikali katika kuwaletea maendeleo wananchi wake.

"Tumeshuhudia taasisi na mashirika ya umma yakitoa gawio la shilingi trilioni 1.3, hizi ni fedha nyingi sana hasa unapoziingiza katika mzunguko wa shughuli za kiuchumi na uboreshaji wa huduma za kijamii, lazima zilete tija katika maisha ya wananchi," amesema Chatanda. 

Sambamba na hilo, Chatanda amesema, mafanikio hayo hayawezi kutenganishwa na uongozi thabiti wa Rais Dk. Samia ambaye daima amekuwa akitoa maelekezo mazuri ya namna bora taasisi hizo zinapaswa kufanya katika kuhakikisha zinazalisha faida na kujitegemea badala ya kuwa tegemezi kwa serikali.

"Rais Dk. Samia amekuwa akizisisitiza taasisi na mashirika ya umma kuzalisha faida na kuepuka utegemezi, kuna baadhi ya taasisi na mashirika yalikuwa hayana uwezo hata wa kutoa gawio, lakini sasa wanatoa gawio baada ya kufanyia kazi maelekezo ya Rais wetu, hivyo, nampongeza sana Rais wetu kwa uongozi wake bora," amesema.

Ikumbukwe kuwa, katika bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027 ya shilingi trilioni 62.3, serikali inatarajia kutumia mapato ya ndani kwa asilimia 74.2 katika utekelezaji wake, hivyo, gawio hili ni sehemu ya kufanikisha utekelezaji wa bajeti ambao ni muhimu katika kufanikisha mipango ya serikali ya maendeleo kwa watu wake.

Naye, Rais Dk. Samia katika hotuba yake, amezielekeza taasisi hizo kuwa wabunifu ili kuongeza tija ya uzalishaji.

"Hatuwezi kujenga uchumi shindani kwa taasisi zinazofanya kazi kwa mazoea. Tunahitaji taasisi zinazopimwa kwa matokeo badala ya takwimu pekee," amesema Rais Dk. Samia.

Kimsingi, gawio na michango ya shilingi trilioni 1.327 kwa mwaka huu ni ongezeko la asilimia 30 kutoka trilioni 1.028 mwaka jana.

Katika kutambua mchango wake, Rais Dk. Samia alitunukiwa Tuzo Maalum ya kuwa "Kinara wa Mageuzi katika Kuimarisha Mifumo ya Usimamizi wa Mashirika ya Umma kwa Maendeleo Jumuishi na Ustawi wa Taifa - Gawio Day 2026".



Na Eva Ngowi, Harare, Zimbabwe

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), ameongoza ujumbe wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Mkutano wa Kamati ya Mawaziri wa Fedha na Uwekezaji wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), unaofanyika jijini Harare, Zimbabwe, ambapo Tanzania imewasilisha msimamo wake kuhusu utekelezaji wa Mfuko wa Maendeleo wa Kikanda wa SADC (SADC Regional Development Fund) pamoja na mapendekezo ya vyanzo mbadala vya kugharamia miradi na programu za maendeleo za kikanda.

Akizungumza baada ya kikao hicho kilichowakutanisha Mawaziri wa Fedha, Magavana wa Benki Kuu na viongozi waandamizi wa sekta za fedha kutoka nchi 16 wanachama wa SADC, Mhe. Luswetula alisema pamoja na kujadili ajenda mbalimbali za maendeleo ya uchumi wa kikanda, Tanzania ilijielekeza katika masuala mawili yenye umuhimu wa kipekee kwa maslahi ya taifa.

Alieleza kuwa suala la kwanza lilihusu utekelezaji wa Mfuko wa Maendeleo wa Kikanda wa SADC, ambapo Tanzania ilieleza kuwa iliridhia mkataba wa Mfuko huo mwaka 2016 na kwa sasa inaendelea kukamilisha taratibu za ndani zitakazoruhusu kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wake.

Aidha, Tanzania ilitoa msisitizo kuwa pamoja na kwamba Mfuko huo ni muhimu katika Ukanda wa SADC, hata hivyo bado kuna changamoto hususan ya upatikaji wa mtaji wa kuanzia kutoka kwa nchi wanachama kutokana na changamoto za kiuchumi walizonazo.

"Tumeeleza kuwa baada ya kukamilika kwa taratibu zote za ndani, Serikali itaijulisha rasmi Sekretarieti ya SADC ili Tanzania iweze kuanza kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa Mfuko wa Maendeleo wa Kikanda," alisema Mhe. Luswetula.

Alisema suala la pili lilihusu mapendekezo ya kutumia tozo za utalii (Tourism Levy) pamoja na ushuru wa forodha (Import levy) kama vyanzo vya kugharamia bajeti, miradi na programu za maendeleo za SADC, ambapo Tanzania ilieleza kuwa mapendekezo hayo yanahitaji kuangaliwa kwa kina zaidi.

Mhe. Luswetula alifafanua kuwa matumizi ya mapato yanayotokana na ushuru wa forodha kwa madhumuni hayo yanakinzana na mfumo wa usimamizi wa mapato nchini Tanzania, kwa kuwa Sheria ya Usimamizi wa Kodi ya mwaka 2015, iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2023, inaelekeza kuwa mapato yote yanayokusanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania yaingizwe katika Mfuko Mkuu wa Serikali.

Aidha, alisema Serikali ya Tanzania imeeleza kuwa matumizi ya tozo za utalii yanaweza kuongeza gharama za utalii nchini, jambo ambalo linaweza kupunguza ushindani wa sekta hiyo na kuathiri jitihada za kuvutia watalii wengi zaidi.

Kutokana na hali hiyo, Tanzania ilipendekeza nchi wanachama ziongeze uwajibikaji kwa kuwasilisha michango yao kwa wakati na kuhakikisha nchi ambazo bado hazijatekeleza wajibu huo wa kimkataba zinatimiza ahadi zao, badala ya kuanzisha tozo mpya zitakazoweza kuathiri uchumi wa nchi wanachama.

"Tunaamini njia endelevu ni kuhakikisha kila nchi inatimiza wajibu wake wa kuchangia bajeti ya SADC kwa wakati ili kuwezesha utekelezaji wa miradi na programu za maendeleo ya kikanda," alisema Mhe. Luswetula.

Mbali na masuala ya sera za fedha, Mhe. Luswetula alisema mkutano huo umeendelea kufungua fursa mpya za biashara na uwekezaji kwa nchi wanachama, huku akiwasihi wafanyabiashara wa Tanzania kutumia ipasavyo soko la SADC lenye nchi 16 na watu zaidi ya million 417 kwa kupanua biashara zao katika sekta mbalimbali, hususan kilimo, biashara na huduma.

Aidha, alibainisha kuwa Tanzania itaendelea kuimarisha sekta ya utalii kwa kutumia fursa zilizopo ndani ya ukanda huo, akieleza kuwa mafanikio yaliyopatikana kupitia kampeni ya Royal Tour iliyoanzishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, yameongeza idadi ya watalii wanaoitembelea Tanzania.

"Kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, tutaendelea kuongeza nguvu katika kuitangaza Tanzania ili iwe kitovu cha utalii barani Afrika," alisema Mhe.Luswetula.

Mkutano huo wa Kamati ya Mawaziri wa Fedha na Uwekezaji wa SADC umejadili masuala mbalimbali ya ushirikiano wa kifedha, uwekezaji, biashara na maendeleo ya kikanda, huku ukilenga kuimarisha ustahimilivu wa uchumi wa nchi wanachama na kuharakisha utekelezaji wa programu za maendeleo chini ya Ajenda ya Maendeleo ya Kikanda ya SADC.

Mkutano huo ulifunguliwa rasmi na Mwenyekiti wa Kamati ya Mawaziri wa Fedha na Uwekezaji wa SADC ambaye pia ni Waziri wa Fedha wa Jamhuri ya Afrika Kusini, Mhe. Enoch Godongwana; ambapo alizitaka nchi wanachama kuimarisha ushirikiano wa kikanda katika kukabiliana na changamoto za uchumi wa dunia, kuendeleza vyanzo endelevu vya ufadhili wa maendeleo, pamoja na kuharakisha utekelezaji wa miradi ya kimkakati itakayochochea ukuaji wa uchumi, biashara na uwekezaji ndani ya ukanda wa SADC.
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), ambaye anaongoza ujumbe wa Tanzania katika Mkutano wa Mawaziri wa Fedha na Uwekezaji wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), akisikiliza kwa makini wakati wa ufunguzi wa mkutano wa maazimio na mapendekezo yaliyofikiwa na vikao vya Makatibu Wakuu wa Hazina, wakati wa vikao vya SADC vinavyoendelea jijini Harare, Zimbabwe.

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), (wa sita kulia) katika picha ya pamoja na Mawaziri wa Fedha na Magavana wa Benki Kuu wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), wakati wa vikaovinavyoendelea jijini Harare, Zimbabwe.

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), (kulia), akifuatilia hotuba ya ufunguzi wa mkutano wa maazimio na mapendekezo wa Mawaziri wa Fedha, Uwekezaji na Afya. Kushoto ni Naibu Waziri Naibu Waziri, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Mhe. Dkt. Pius Chaya (Mb).

Ujumbe kutoka Tanzania ukifuatailia ufunguzi wa mkutano wa Mkutano wa Mawaziri wa Fedha na Uwekezaji wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC unaoendelea Harare nchini Zimbabwe.

Mkutano wa Kamati ya Mawaziri wa Fedha na Uwekezaji wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), unaofanyika mjini Harare, Zimbabwe, ukiwakutanisha Mawaziri wa Fedha, Magavana wa Benki Kuu na Maafisa Waandamizi wa Hazina kutoka nchi wanachama.


Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), (kulia) akifurahia jambo wakati wakibadilishana Mawazo na Balozi wa Tanzania nchini Zimbabwe Mhe, CP Suzan Kaganda, (kushoto) pamoja na Mkurugenzi wa Kanda ya Afrika wa Shirika la Afya Duniani – WHO, Prof. Mohamed Yakub Janabi wakati wa mapumziko ya Vikao vya Mikutano ya Kamati ya Mawaziri wa Fedha na Uwekezaji wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) inayoendelea Harare nchini Zimbabwe.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha)




Top News