NA MWANDISHIWI WETU – MASVINGO – ZIMBABWE

Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Kaspar Mmuya (Mb), amewasili nchini Zimbabwe kushiriki Mkutano wa Sita (6) wa Kawaida wa Kamati ya Mawaziri Wanaohusika na Usimamizi wa Maafa kwa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu Mheshimiwa Profesa Palamagamba Kabudi unaofanyika Masvingo, Zimbabwe kuanzia tarehe 11 haadi 14 Mei, 2026.

Mara baada ya kuwasili, Mhe. Mmuya amepokelewa na Balozi wa Tanzania nchini humo, Mhe. Balozi Suzan S. Kaganda na kuipongeza Tanzania kushiriki katika mkutano huo unaolenga kujadili maendeleo yaliyopatikana katika utekelezaji wa programu za kikanda na masuala ya kimkakati katika utekelezaji wa afua mbalimbali katika Usimamizi wa maafa kwa nchi za SADC.

Masuala mengine yaliyoelezwa na Mheshimiwa Balozi Suzani ni  pamoja na Tanzania kuendelea kuzitangaza fursa zilizopo ikiwemo sekta ya utalii, uchukuzi pamoja na kilimo  huku akiahidi kuendelea kuimarisha ushirikiano uliopo baina ya Tanzania na Zimbabwe.

Sambamba na hayo, mkutano huo utahudhuriwa na wadau mbalimbali wa masuala ya Usimamizi wa Maafa kutoka Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) ambapo ni fursa kwa Tanzania kuendelea kujitangaza Kimataifa kwa kuwa na mifumo thabiti ya Usimamizi wa Maafa pamoja na  kubadilishana uzoefu kuhusu masuala ya Menejimenti ya maafa.

Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizoshiriki katika Mkutano huo wa siku Nne ambapo umekutanisha wadau wa  masuala ya maafa kutoka nchi kumi na sita wakiwemo wataalamu kutoka  katika ngazi za Kimataifa pamoja na Mashirika ya Umoja wa Kimataifa.








Na Janeth Raphael MichuziTv

Serikali imeendelea kuimarisha sekta ya afya nchini kwa kuongeza ajira za watumishi wa kada mbalimbali, hatua inayolenga kupunguza uhaba wa wataalamu katika hospitali, vituo vya afya na zahanati, hususan katika maeneo yenye upungufu mkubwa wa watumishi.

Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Dkt. Jafar Seif, amesema katika kipindi cha mwaka wa fedha 2020/21 hadi 2025/26 Serikali imeajiri jumla ya watumishi 37,921 wa kada za afya na kuwapangia vituo vya kazi katika Mamlaka za Serikali za Mitaa nchini.

Dkt. Seif ametoa kauli hiyo bungeni leo wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Christina Solomon Mndeme, aliyetaka kufahamu mkakati wa Serikali wa kuongeza watumishi wa afya katika Mkoa wa Tabora ili kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Akizungumzia hali ya Mkoa wa Tabora, Dkt. Seif amesema mahitaji halisi ya wataalamu wa afya ni watumishi 8,121, lakini waliopo sasa ni 3,467 pekee, sawa na asilimia 43 ya mahitaji yote. Hivyo, mkoa huo bado unakabiliwa na upungufu wa watumishi 4,654, sawa na asilimia 57.

Amesema licha ya changamoto hiyo, Serikali imeendelea kuchukua hatua za kupunguza pengo hilo ambapo kati ya mwaka wa fedha 2024/25 hadi 2025/26, jumla ya watumishi 856 wa kada mbalimbali za afya wameajiriwa na kupangiwa vituo vya kazi katika halmashauri zote za Mkoa wa Tabora.

Aidha, Dkt. Seif amesema halmashauri nane za Mkoa wa Tabora zimeandaa mkakati maalum wa kuongeza nguvu kazi katika sekta ya afya kupitia mapato ya ndani. Kwa mwaka wa fedha 2026/27, halmashauri hizo zimetenga jumla ya shilingi milioni 413.8 kwa ajili ya kuajiri watumishi 87 wa afya kwa mfumo wa mikataba.

Kwa mujibu wa Serikali, hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za afya karibu na maeneo yao pamoja na kupunguza mzigo wa kazi kwa watumishi waliopo sasa katika vituo vya kutolea huduma.

Serikali imeendelea kusisitiza kuwa itaendelea kuboresha mazingira ya utoaji huduma za afya nchini kwa kuongeza ajira, kuimarisha miundombinu ya afya na kuhakikisha wataalamu wa kutosha wanapatikana katika maeneo yenye uhitaji mkubwa.





Viongozi mbalimbali wa Chama cha mapinduzi Mkoa na Wilayani wakiambatana na Viongozi wa Serikali mkoa wa Dodoma wameanza safari ya Kikazi kuelekea mkoani Mtwara kwenye Vyama Vikuu na Vyama vya Ushirika vya Msingi.

Viongozi hao wakingozana na Mrajis Msaidizi wa mkoa wa Dodoma Ndg Joseph Chitinka na Mwenyekiti wa Chama Kikuu cha Ushirika mkoa wa Dodoma Bibi Theresia Nyoka wameanza ziara hiyo leo Mei 12, 2026 kutokea mkoani Dodoma kuelekea mkoani humo.

Mrajis Msaidizi wa mkoa wa Dodoma ameeleza lengo la ziara hiyo ni kuwajengea uwezo, kujifunza utekelezaji wa Mfumo wa stakabadhi za ghala na kujionea utekelezaji wa miradi mbalimbali kwenye Vyama Vikuu na Vyama vya Msingi Ushirika vya mkoa wa Mtwara na hivyo kurahisisha utekelezaji wa majukumu ya kiushirika ndani ya Mkoa wa Dodoma.

Ziara hiyo inafanyika kwa muda wa siku mbili kuanzia Mei 13 hadi 14, 2026 na kuwahusisha Wajumbe wa Kamati ya Siasa Mkoa, Wenyeviti wa CCM Wilaya Mkoani Dodoma, Sekretariti ya Mkoa CCM, Baadhi ya Makatibu wa Chama wilaya na Wenezi,, Makatibu, Makatibu Tawala Uchumi na Uzalishaji Viwanda na Biashara na Kilimo.

Na Munir Shemweta, MASASI

Mbunge wa Jimbo la Mtwara Mjini ambaye pia ni Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo ameahidi kukiunga mkono kikundi cha vijana cha UBINAKI kinachojishughulisha na mradi wa utengemezaji samani za majumbani na ofisini.

Mradi wa vijana wa UBINAKI unatokana na mkopo wa asilimia 10 unaotolewa na Halmashauri kwa makundi ya vijana, wanawake pamoja na watu wenye walemavu ambapo vijana hao wa Masasi wameonesha ubunifu mkubwa pamoja na matumizi sahihi ya fedha walizopatiwa kwa kuanzisha shughuli yenye tija kwao na kwa jamii inayowazunguka.

Akizungumza wakati wa ukaguzi wa mradi wa vijana wa UBINAKI wakati wa Mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa jana katika halmashauri ya Mji Masasi Dkt Akwilapo amewapongeza vijana hao kwa kuungana, kufanya kazi pamoja sambamba na kujitegemea katika kuendesha shughuli za kujitafutia kipato.

‘’Hawa ni mfano wa kuigwa na ningependa vijana wengine wote waige mfano wa vijana hawa na mimi hawa nitawaunga mkono’’ amesema Mhe. Dkt Akwilapo

Katika kuonesha dhamira ya kuwawezesha vijana hao, Mhe. Dkt Akwilapo aliahidi kununua kitanda kimoja kati ya vile vilivyotengenezwa na vijana hao ikiwa ni ishara ya kuwaunga mkono.

Aidha, aliwaambia vijana hao wa UBINAKI kuwa, katika ile pesa wanaorejesha mkopo wa asilimia 10 wa halmashauri ya Mji Masasi atawachangia kiasi cha shilingi laki nne katika kipindi cha miezi sita ya marejesho.

Amesema, uamuzi wa kuwasaidia vijana hao ni kuongeza hamasa kwa vijana wengine kuanzisha vikundi kama hivyo na yeye atawaunga mkono kwa sababu uanzishwaji vikundi vya aina hiyo utawafanya vijana kujitegemea, kuwa na kazi na kuacha kutumia muda mwingi katika michezo ya pool table na mambo mengine yasiyo na faida.

Kwa mujibu wa taarifa ya kikundi cha UBINAKI, mafanikio makubwa yaliyopatikana ndani ya kikundi hicho ni pamoja na vijana kujiajiri kupitia shughuli za utengenezaji na uuzaji wa samani, kupata soko la bidhaa za ndani ya mkoa wa Mtwara na nje ya Mkoa pamoja na kutoa ajira kwa vijana 8.

Kikundi cha Vijana cha UBINAKI kilianzishwa tarehe 21.03.2023 kikiwa na mtaji wa shilingi 3,380,000 ikijumuisha na mashine za mkono ambazo zilitokana na michango toka kwa wanakikundi. Kikundi kilipata usajili kwa namba MTW/MAS/VIJ/2023/0044 kikiwa na wanachama 5(1Ke na 4 Me).

Halmashauri ya Mji Masasi ilikipatia mkopo wa Shilingi 30,972,000/= kikundi cha UBINAKI kupitia fedha za asilimia 10% ya mapato ya ndani. Mkopo huo umekisaidia kikundi cha vijana hao kuboresha mazingira ya kiwanda, ununuzi wa Malighafi, vitendea kazi ikiwemo Kununua mashine za kisasa mbili (2).

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akizungumza wakati wa ukaguzi wa mradi wa Kikundi cha Vijana cha UBINAKI uliofanywa wakati wa Mbio za Mwenge kitaifa katika halmashauri ya Mji Masasi mkoani Mtwara jana.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akiangalia sehemu ya Samani zilizotengenezwa na kikundi cha vijana cha UBINAKI wakati wa ukaguzi wa mradi wa Kikundi hicho uliofanywa wakati wa Mbio za Mwenge wa Uhuru katika halmashauri ya Mji Masasi mkoani Mtwara jana.

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa mwaka 2026 Bw. Michael Mwang’onda akipata maelezo ya mradi wa utengenezaji Samani unaofanywa na Kikundi cha Vijana cha UBINAKI wakati wa ukaguzi wa mradi wa Kikundi katika halmashauri ya Mji Masasi mkoani Mtwara jana. Wa tatu kulia ni Mbunge wa jimbo la Masasi Mjini na Waziri wa Ardhi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo.

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa mwaka 2026 Bw. Michael Mwang’onda akizungumza wakati wa ukaguzi wa mradi wa utengenezaji Samani unaofanywa na Kikundi cha Vijana cha UBINAKI katika halmashauri ya Mji Masasi mkoani Mtwara jana.

Na. Aron Msigwa - Nairobi, Kenya.

Mkurugenzi wa Mafunzo na Elimu ya Jumla ya Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Kanali Beno Mathias Nzowa amesema Tanzania imejipanga kikamilifu kushiriki zoezi la pamoja la 14 la Vituo vya Uamrishaji vya Kijeshi vya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) - Ushirikiano Imara 2026, litakalofunguliwa rasmi Mei 14, 2026 katika viwanja vya Ulinzi Sports Complex jijini Nairobi, Kenya.

Kanali Nzowa amesema hayo baada ya kutembelea kikundi cha Tanzania kinachoshiriki zoezi hilo katika Kituo cha Mafunzo cha Masuala ya Usalama na Haki za Binadamu (HPSS) jijini Nairobi kwa lengo la kukagua maandalizi na utayari wa washiriki kuelekea uzinduzi rasmi wa zoezi hilo la kikanda lililowajumuisha Maofisa  wa Jeshi, Polisi, Magereza, Uhamiaji, Zimamoto,Wizara na taasisi za kiraia  .

“Nimekuja hapa kuangalia maandalizi kuelekea ufunguzi wa zoezi ambalo litafanyika kwa siku 14. Maandalizi ni mazuri na Kikosi chetu kutoka Tanzania kina utayari mkubwa pamoja na morali ya hali ya juu kutokana na maandalizi na mafunzo ya awali yaliyoelekezwa na Mkuu wa Majeshi kufanyika jijini Arusha,” amesema Kanali Nzowa.

Zoezi la Ushirikiano Imara 2026 linawakutanisha washiriki kutoka Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa kijeshi, usalama wa kikanda pamoja na uwezo wa kukabiliana na changamoto mbalimbali za kiusalama.







 


UBORA wa rasilima watu( Afya na Maarifa) ndio sarafu ya dunia kwa sasa na hivyo kete muhimu kwa Tanzania kujiunga na Mataifa tajiri mwaka 2050( Trilioni dola Club).

Wauguzi ndio Nguzo ya Rasilimali Watu na Mhimili wa Uchumi wa Dola Trilioni 1 (2050)

Katika Maadhimisho ya Siku ya Wauguzi Duniani, tunatambua kuwa uuguzi si kazi tu, bali ni wito wa kitume unaohitaji upendo, subira, na utu wa hali ya juu. Wauguzi ni daraja kati ya wagonjwa na kupona, wakiwa mstari wa mbele kuokoa maisha.

Bila afya bora, hakuna tija kazini; wauguzi wanahakikisha jamii ina afya, na hivyo kuwa kiungo muhimu kimkakati katika kujenga uchumi mkubwa.

Tanzania inalenga kujiunga na "Club" ya nchi zenye uchumi wa kuanzia dola trilioni moja ifikapo 2050. Hata hivyo, ili kufika huko, tunahitaji rasilimali watu yenye afya bora.

Pamoja na uwekezaji mkubwa wa kibajeti kuboresha miundomibinu ya huduma, vifaa tiba, dawa, wauguzi na madaktari uliofanywa na Serikali, Bado kuna changamoto kubwa ya uwiano idadi ya wauguzi kwa idadi ya watu.Wakati WHO inapendekeza uwiano wauguzi kwa idadi ya watu kuwa wauguzi 45 kwa watu 10,000, Afrika kwa wastani bado ipo chini sana ikiwa na wastani wa wauguzi 18 kwa watu 10,000. Huku nchi tajiri duniani, zimefika uwiano wa wauguzi100 kwa watu 10,000.

Hii inamaanisha uwekezaji wetu katika uuguzi lazima uongezeke mara dufu kuelekea kujiunga na nchi hizo kama tulivyokubaliana kwenye Dira2050, Na kufikia hilo hatuwezi kutegemea serikali pekee.

Mchango wa sekta binafsi ni muhimu sana:Takwimu zinaonesha Sekta binafsi nchini Tanzania inatarajiwa kuchangia asilimia 70 (Tsh Trilioni 334) ya gharama za Mpango wa Maendeleo wa Taifa ifikapo 2026/27- 2030/31.

Zaidi ya asilimia 50 ya matumizi ya afya yanachangiwa na sekta binafsi, na takriban 40% ya vituo vya afya vinamilikiwa au kuendeshwa na sekta binafsi nchini.

Changamoto ya sekta hii ni mtambukwa, Na ina wajibu wa pande zote. Kwa upande wa Serikali ni kuendelea kuimarisha Ubia kati yake na Sekta Binafsi na dhana nzima ya uwekezaji kama inavyosisitizwa na Rais wetu Dr SSH, lakin kwa upande wa wananchi ni kutekeleza uzazi wa Mpango kwani kuna uhusiano mkubwa kati ya umasikini na kasi ya ongezeko la watu hasa katika nchi masikini ambazo uwezo wa serikali kutoa afya na elimu bora kwa kaya masikini bado changamoto kubwa.

Nikatika juhudi za kuongeza uwezo wa kugharimia sekta muhimu kama Afya na Elimu kwa masikini, tunaendelea kusisitiza PPP ili Serikali iendelee kuachana na kuwekeza maeneo yenye mvuto wa sekta binafsi na inachokiokoa kisaidie maeneo kama afya kwa masikini ambayo hayana mvuto kwa Sekta Binafsi kwakuwa hayalipi kibiashara lakin ni muhimu kwa uchumi na ustawi wa Taifa.

Wauguzi ndio uhai wa sekta ya afya. Uwekezaji katika wauguzi ni uwekezaji katika uchumi wetu.

Kazi ya kipekee ya muuguzi ni kumsaidia mtu, mgonjwa au mzima, katika kufanya shughuli zile zinazochangia afya au kupona (au kifo cha amani), ambazo angeweza kufanya bila kusaidiwa kama angekuwa na nguvu, utashi, au maarifa ya kutosha. Heri ya Siku ya Wauguzi. Changamoto ni nyingi lakini lipo tumaini kadiri tunavyojenga na kufungua uchumi! Upo uhusiano mkubwa kati ya ukubwa wa uchumi na ubora wa maisha ya wauguzi
Na Mwandishi Wetu
KUELEKEA msimu mwingine wa Tamasha la Kyela Ibhasa Festival linalofanyika kila mwisho wa mwaka wilayani Kyela mkoani Mbeya, kikundi cha wazawa wa Kyela kiitwacho Bhalondo kimeweka rekodi mpya ya uchangiaji baada ya kufanikisha kukusanya shilingi milioni 2.85 kwa ajili ya maandalizi ya tamasha hilo.

Rekodi hiyo imekuwa ya kipekee tangu kuanzishwa kwa umoja huo, huku kikundi hicho chenye wanachama 19 kikionekana kuwa mfano wa kujitolea na mshikamano katika kuendeleza shughuli za kijamii na maendeleo ya nyumbani kwao.

Kwa mujibu wa wanakikundi hao, mafanikio hayo yametokana na utaratibu waliouweka wa kuchanga fedha kila mwisho wa mwezi kwa lengo la kuhakikisha kabla ya mwezi Juni tayari wanakuwa wamemaliza mchango wao, ili muda unaobaki uwe wa kujipanga zaidi kwa ajili ya kufanikisha tamasha hilo litakalofanyika mwezi Desemba mwaka huu.

Mtunza Hazina wa kikundi hicho, Janeth Mophaty, amesema siri ya mafanikio yao ni moyo wa uzalendo na dhamira ya dhati ya kuipenda Kyela pamoja na kutambua kuwa maendeleo ya tamasha hilo yanahitaji watu kujitoa kwa hali na mali.

“Tumekuwa na ushirikiano mkubwa ndani ya kikundi chetu. Kila mmoja ameonyesha dhamira ya kuona Kyela Ibhasa Festival inakuwa kubwa zaidi mwaka hadi mwaka. Ndiyo maana tumeweza kuvunja rekodi na kumaliza mchango wetu mapema,” amesema Janeth.

Amesema tamasha hilo limeendelea kuwa chachu ya kuwakutanisha wana Kyela waliopo ndani na nje ya nchi, sambamba na kutangaza utamaduni, utalii na fursa mbalimbali za kiuchumi zilizopo wilayani humo.

Ikumbukwe kuwa , Umoja wa Kyela Ibhasa Festival umeweka utaratibu wa kila mwana Kyela kuchangia kuanzia shilingi 150,000 na kuendelea, kwa ajili ya kuhakikisha maandalizi ya tamasha hilo yanafanikiwa kama ilivyokusudiwa.


Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Wakati Tanzania ikiendelea kukabiliwa na changamoto ya ongezeko la taka ngumu mijini na vijijini, Serikali imezitaka halmashauri zote nchini kuhakikisha mapato yatokanayo na shughuli za usafi na udhibiti wa taka yanatumika moja kwa moja kuboresha huduma hizo pamoja na kuimarisha mazingira.

Hatua hiyo inalenga kuongeza ufanisi wa ukusanyaji na usimamizi wa taka huku Serikali ikihimiza jamii kuanza kuzitazama taka kama rasilimali yenye thamani ya kiuchumi badala ya mzigo wa mazingira.

Akizungumza leo Mei 12, 2026 jijini Dodoma wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Mwaka wa Tathmini ya Utekelezaji wa Afua za Udhibiti wa Taka Ngumu na Usafi wa Miji, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Profesa Riziki Shemdoe amesema halmashauri zote zinapaswa kutenga na kurejesha asilimia 10 ya mapato yanayotokana na shughuli za udhibiti wa taka ili kuviwezesha vitengo vya usafi wa mazingira kufanya kazi kwa ufanisi zaidi.

Mkutano huo umebeba kaulimbiu isemayo “Taka Ngumu ni Mali; Tumia, Rejeleza na Weka Miji Safi.”

Profesa Shemdoe amesema bado hali ya usimamizi wa taka nchini si ya kuridhisha kutokana na baadhi ya halmashauri kushindwa kuwa na maeneo rasmi ya kutupia taka.

Amesema kati ya halmashauri 184 zilizopo nchini, ni halmashauri 43 pekee zenye madampo rasmi, jambo ambalo linaathiri juhudi za usafi wa mazingira na kuongeza hatari ya uchafuzi wa mazingira pamoja na magonjwa ya mlipuko.

“Ni muhimu kuhakikisha taka zinakusanywa na kuhifadhiwa katika maeneo maalum ili kulinda afya za wananchi na kuweka mazingira safi katika miji na makazi yetu,” amesema.

Aidha, ameonya kuhusu tabia ya utupaji holela wa taka kwenye mitaro ya maji, akisema hali hiyo imekuwa chanzo kikubwa cha mafuriko wakati wa mvua kutokana na kuziba kwa mifumo ya maji.

Kwa mujibu wa Profesa Shemdoe, viongozi wa mikoa, wilaya pamoja na serikali za mitaa wanapaswa kuhakikisha suala la usafi wa mazingira linakuwa agenda ya kudumu katika vikao vya maamuzi ili kuongeza uwajibikaji katika jamii.

Katika hatua nyingine, Serikali imehimiza wananchi kuanza kutenganisha taka kuanzia zinakozalishwa ili kurahisisha shughuli za urejelezaji wa plastiki, vyuma, karatasi na taka nyingine zinazoweza kutumika tena.

Amesema mfumo huo utasaidia kuongeza thamani ya taka na kufungua fursa mpya za ajira na biashara kwa wananchi, hususan vijana na wanawake.

“Tunapaswa kubadili mtazamo kuhusu taka. Zinaweza kuwa chanzo kikubwa cha kipato kupitia shughuli za ukusanyaji, uchakataji na urejelezaji,” amesema.

Profesa Shemdoe pia amewataka vijana na wanawake kutumia mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri kuanzisha miradi ya ukusanyaji na uchakataji wa taka ngumu ili kujiongezea kipato huku wakichangia uhifadhi wa mazingira.

Amesema Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan inaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo ikiwemo Japan kutafuta teknolojia za kisasa za uteketezaji na urejelezaji wa taka kwa lengo la kupata suluhisho la kudumu la usimamizi wa taka nchini.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule amesema Mkoa wa Dodoma umeongeza bajeti ya usafi wa mazingira kutoka Shilingi milioni 750 hadi Shilingi bilioni 3 kwa mwaka wa fedha 2026/27.

Amesema fedha hizo zitatumika kununua vifaa vya usafi, kuboresha ukusanyaji wa taka pamoja na kutoa elimu kwa wananchi kuhusu utunzaji wa mazingira.

Naye Mkurugenzi Msaidizi wa Sehemu ya Mabadiliko ya Tabianchi na Tathmini kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, Dk. Kanizio Manyika amesema Tanzania huzalisha zaidi ya tani milioni 17 za taka ngumu kila mwaka huku asilimia 60 hadi 75 ya taka hizo zikibaki kwenye mazingira kutokana na kutokusanywa ipasavyo.

Ameonya kuwa hali hiyo ni tishio kwa afya za wananchi na mazingira na kusisitiza umuhimu wa kuwa na mifumo endelevu ya usimamizi wa taka.

Kwa upande wake, mwakilishi kutoka Wizara ya Afya, Joseph Birango amesema takwimu zinaonyesha magonjwa sita kati ya 10 yanayoisumbua jamii yanachangiwa na uchafuzi wa mazingira pamoja na mifumo duni ya usimamizi wa taka.

Awali, Mwenyekiti wa Wakuu wa Vitengo vya Udhibiti wa Taka na Usafi wa Mazingira Tanzania Bara, William Mpangala aliitaka Serikali kutoa maelekezo madhubuti zaidi kwa halmashauri ili kuhakikisha fedha zinazotokana na shughuli za udhibiti wa taka zinarejeshwa kikamilifu katika kuboresha huduma za usafi wa mazingira.







*Rais Macron atangaza uwekezaji wa dola bilioni 27 Barani Afrika

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Mei 11, 2026 ameshiriki katika ufunguzi wa Mkutano wa Ushirikiano kati ya Afrika na Ufaransa (Africa Forward: Africa–France Partnership for Innovation and Growth Summit) unaofanyika jijini Nairobi, Kenya.

Mkutano huo umewakutanisha Wakuu wa Nchi na Serikali, viongozi wa sekta binafsi, wadau wa maendeleo pamoja na wawekezaji kwa lengo la kuimarisha ushirikiano kati ya Afrika na Ufaransa katika sekta mbalimbali ikiwemo biashara, teknolojia, nishati, afya, Akili Unde (AI), kilimo, uchumi wa buluu pamoja na viwanda.

Akizungumza baada ya mkutano huo, Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amesema mkutano huo umekuwa wa manufaa kwa Bara la Afrika na Ufaransa kwa pamoja kwani majadiliano yamegusa namna ya kuzifanya pande hizo mbili ziweze kunufaika na ushirikiano huo.

Amesema rasilimali zinazopatikana barani Afrika zinatosheleza ikiwa zitatumika vizuri katika kujenga uchumi wa Afrika.

“Lengo kubwa la jitihada hizi ni kupambana na umasikini lakini pia na kutengeneza ajira kwa makundi makubwa ikiwemo la vijana pamoja na wanawake,” amesema.

Aidha, Waziri Mkuu amesema maeneo mengi yaliyojadiliwa ni maeneo ambayo yamepewa umuhimu katika Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050.

“Nguzo zote zilizoongelewa kwenye dira lakini pia na maeneo ya kipaumbele yameguswa katika mijadala ya leo,” amesema.

Akizungumza katika mkutano huo, Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mheshimiwa Dkt. William Samoei Ruto, alizitaka nchi za Afrika kutafakari upya mifumo ya kiuchumi kwa kuimarisha ukusanyaji wa rasilimali za ndani, uwekezaji pamoja na ushirikiano wa kikanda ili kuhakikisha kunakuwa na maendeleo ya muda mrefu.

Aidha, Rais Ruto amesema ni wakati wa Afrika kujiweka kama mdau katika uchumi wa kimataifa badala ya kuwa mnufaika wa misaada ya nje pekee.

“Afrika haiwezi tena kubaki kama mshiriki asiyekuwa na sauti katika mifumo ya kimataifa ambapo baadhi ya maamuzi muhimu hufanywa bila sauti ya usawa,” alisema.

Kwa upande wake, Rais wa Jamhuri ya Ufaransa, Mheshimiwa Emmanuel Macron, alisema Bara la Afrika linapiga hatua kubwa za maendeleo na ni bara ambalo halisubiri majawabu ya changamoto bali linatoa majawabu ya changamoto mbalimbali lilazokabiliana nazo.

Katika hatua nyingine, Rais Macron alitangaza uwekezaji wa thamani ya dola za Marekani bilioni 27 barani Afrika katika sekta za nishati, Akili Unde, uchumi wa bahari pamoja na kilimo.

“Mpango huu utasaidia kutengeneza takriban ajira 250,000 barani Afrika na nchini Ufaransa,” alisema.

Aidha, Rais Macron aliwataka wafanyabiashara wa Afrika kuona fursa zilizopo nchini Ufaransa na kwenda kuwekeza.

“Hatuko hapa tu kuja kuwekeza katika Bara la Afrika pamoja nanyi, tunawahitaji viongozi wakubwa wa biashara wa Afrika kuja kuwekeza nchini Ufaransa,” alisema.

Kwa Upande wake Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres alisema watu wa Bara la Afrika wanapaswa kuwa wa kwanza kunufaika na rasilimali za bara hilo.

“Bara hili limebarikiwa rasilimali nyingi, hapa wenyewe ndio wanapaswa wawe wa kwanza kunufaika,” alisema.

Dkt. Mwigulu amemuwakilisha Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika mkutano.


Na Mwandishi wetu, Simanjiro
JUMUIYA ya Wazazi wa CCM Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara, imesajili wanachama wapya 16,648 kwa njia ya kielekroniki.

Katibu wa jumuiya ya wazazi wa CCM wilaya ya Simanjiro, Sasi Mirumbe ameeleza hayo kwenye kilele cha maadhimisho ya wiki ya wazazi iliyofanyika kata ya Ruvu Remit.

Mirumbe amesema kuwa kati ya wanachama hao wapya 16,648 wanaume ni 7,319 na wanawake ni 9,165.

Ameeleza kwamba katika uhai wa jumuiya hiyo wamekuwa wakifanya vikao na ziara kwa mujibu wa kanuni na kusajili wanachama wapya.

Amesema kutokana na jumuiya ya wazazi kuhusika na mazingira, malezi ya vijana katika elimu afya na uchumi wa kujitegemea, jukumu ambalo wamekuwa wakilifanya mara kwa mara na vizuri sana.

"Tumekwenda mbali kama jumuiya ya wazazi Simanjiro kwa kutambua baadhi ya watu wazima wasiojua kusoma na kuandika tumekuja na mpango wa darasa mabomani," amesema Mirumbe.

Amesema darasa mabomani ni mpango wa kuwafundisha watu wazima kwenye vitongoji vyao majumbani ili wajue kusoma, kuhesabu na kuandika, kwa kutoa mchango wao wa elimu ya awali, msingi na sekondari kama wazazi.

Amesema ujenzi wa nyumba ya mtumishi, wamefanikiwa kuanza ujenzi ambayo hivi sasa ipo usawa wa madirisha.

"Mhe mgeni rasmi kukamilika kwa nyumba hii kutaendelea kuimarisha jumuiya yetu na chama chetu katika kuongeza rasilimali za kudumu na kupunguza adha kwa mtumishi kupanga pindi yakitokea mabadiliko ya kiutumishi, amesema.

Aidha, amesema nyumba hiyo imesimama kwa muda wa mwaka mmoja kwa kukosa matofali 1,000 ya thamani ya shilingi milioni 1.4 saruji mifuko 50 ya shilingi 900,000 nondo za mm12 shilingi milioni 1 nondo za mm6 za shilingi milioni 1.4 misumari ya shilingi 17,000 mbao shilingi 540,000 binding wire sh 70,000 fedha za fundi shilingi 1.6 jumla shilingi 5,747,500.

Mgeni rasmi wa maadhimisho hayo James Ole Millya ameipongeza jumuiya hiyo kwa namna wanavyotekeleza wajibu wao ikiwemo kuyasema mema yanayofanywa na Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan.

Ole Millya amechangia shilingi 500,000 za ujenzi wa nyumba ya mtumishi na kumuagiza mfanyabiashara maarufu Lesiangiki Mulla kushirikiana na wadau wa maendeleo kukamilisha jengo hilo.

Mwenyekiti wa jumuiya ya wazazi wa CCM Wilaya ya Simanjiro, Haiyo Yamat Mamasita amesema wamekuwa na utaratibu wa kufanya maadhimisho ya wiki ya wazazi katika kata mbalimbali.

Haiyo amesema kwa mwaka 2026 waliamua kupitia vikao kuwa kilele cha maadhimisho hayo yafanyike kata ya Ruvu Remit na mwaka 2027 yatafanyika katika kata nyingine.

 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) inatarajia kutoa vibali vya ajira mpya katika mwaka wa fedha 2026/27 kwa sekta ya afya pamoja na kada nyingine, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kupunguza uhaba wa madaktari na wauguzi nchini.
 Akizungumza Mei 12, 2026 katika Kongamano la Kwanza la Kisayansi la Wauguzi lililoambatana na Maadhimisho ya Siku ya Wauguzi Duniani yaliyofanyika katika Hotel Verde Zanzibar, Rais Dkt. Mwinyi alisema Serikali itaendelea kuwekeza zaidi katika kuboresha huduma za afya ili kuhakikisha wananchi wanapata matibabu bora na ya kisasa.
 Alieleza kuwa Serikali inaendelea na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya afya ikiwemo ujenzi wa Hospitali Mpya ya Mnazi Mmoja pamoja na Hospitali ya Saratani Binguni, sambamba na ununuzi wa vifaa tiba vya kisasa na kuimarisha mafunzo kwa watumishi wa sekta hiyo.

 Rais Dkt. Mwinyi pia aliwataka wauguzi nchini kuendelea kufanya kazi kwa kujituma, huruma na kuzingatia maadili ya taaluma yao, akisisitiza kuwa wauguzi wana nafasi kubwa katika kuimarisha huduma za afya na kuokoa maisha ya wananchi.
 Maadhimisho ya Siku ya Wauguzi Duniani mwaka huu yamebeba kauli mbiu isemayo, “Kuwawezesha Wauguzi ni Kuokoa Maisha” (Empowering Nurses, Saving Lives).


Na mwandishi wetu
WAZIRI wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Angellah Kairuki, amewataka waandishi wa habari pamoja na jamii kwa ujumla kutambua wajibu wao katika kusimamia malezi na makuzi ya watoto ili kujenga familia imara na taifa lenye maadili mema.

Akizungumza katika semina ya malezi iliyoandaliwa na Wizara ya Maendeleo ya Jamii na Makundi Maalum Kairuki alisema mafanikio ya kibiashara, kiuongozi na kijamii hayawezi kuwa na maana endapo msingi wa familia katika malezi na makuzi haujajengwa vizuri.

“Tutambue hivyo, pamoja na yote utafanikiwa kibiashara, kiuongozi na mengine mengi lakini kama msingi wa familia yako katika malezi na makuzi haujakaa sawa utateteleka. Hata ukipata mafanikio yatakuwa ya muda mfupi na hutakuwa na faraja wala furaha, hivyo eneo hili ni la kusisitiza na kutilia mkazo,” alisema Kairuki.

Aidha, aliitaka jamii kuzingatia matumizi sahihi ya simu za mkononi pamoja na vyombo vingine vya teknolojia, akieleza kuwa watoto wengi wamejikuta wakitumia vibaya mitandao ya kijamii.

“Kwa mujibu wa sheria na kanuni za nchi, laini ya simu hutolewa kwa mtu mwenye umri wa miaka 18 kwenda juu. Sasa unabaki na maswali unapoambiwa watoto wetu wameona vitu vya hovyo, unajiuliza wanavionea wapi ilhali kanuni zinakataza,” alisema.

Kairuki alisisitiza kuwa mtoto hastahili kumiliki simu ya mkononi, huku akibainisha kuwa baadhi ya wazazi na walezi wamelegeza usimamizi wao jambo linalochangia watoto kuathirika na matumizi mabaya ya teknolojia.

“Ni muhimu kwa wazazi kutambua kuwa sheria za nchi haziruhusu jambo hilo, hivyo niwaombe sana kutambua kuwa ulinzi unaanza na sisi wenyewe majumbani mwetu kwa kufuatilia watoto wetu wanaangalia nini chini ya ulinzi wetu,” alisisitiza.

Katika hatua nyingine, Kairuki alikemea tabia ya matusi, udhalilishaji na matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii, akisema vitendo hivyo ni kosa kisheria na vyombo vya dola vitaendelea kuchukua hatua dhidi ya wanaokiuka sheria.

“Vyombo vya ulinzi na usalama vitaendelea kusimamia suala hili ikiwemo kufunga akaunti mbalimbali za watu watakaokiuka sheria. Mitandao ina fursa nyingi chanya kwa maendeleo binafsi na jamii hivyo itumike kwa manufaa,” alisema.

Naye Daktari wa Saikolojia ya Jamii, Dkt. Garvin Kweka alisema wazazi wengi kwa sasa wanalea watoto wasioweza kuhimili changamoto za maisha pamoja na hisia zao.
“Ndiyo maana siku hizi watoto wameanza kujiua. Hii ni kutokana na kutengeneza kizazi kisichoweza kuhimili maumivu kabisa. Nina takwimu kuwa mtoto wa kwanza mwenye umri mdogo kujiua alikuwa na miaka sita kutoka Mkoa wa Katavi,” alisema.

Aliongeza kuwa jamii inapaswa kuwajengea watoto uwezo wa kukabiliana na changamoto za maisha badala ya kuwalea katika mazingira yanayowafanya washindwe kuvumilia misukosuko mbalimbali ya maisha.

▪️Dkt. Mwigulu asisitiza matumizi sahihi ya rasilimali ili kujenga uchumi wa Afrika

▪️Rais Macron atangaza uwekezaji wa dola bilioni 27 Barani Afrika
 
WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Mei 12, 2026 ameshiriki katika ufunguzi wa Mkutano wa Ushirikiano kati ya Afrika na Ufaransa (Africa Forward: Africa–France Partnership for Innovation and Growth Summit) unaofanyika jijini Nairobi, Kenya.
 
Mkutano huo umewakutanisha Wakuu wa Nchi na Serikali, viongozi wa sekta binafsi, wadau wa maendeleo pamoja na wawekezaji kwa lengo la kuimarisha ushirikiano kati ya Afrika na Ufaransa katika sekta mbalimbali ikiwemo biashara, teknolojia, nishati, afya, Akili Unde (AI), kilimo, uchumi wa buluu pamoja na viwanda.
 
Akizungumza baada ya mkutano huo, Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amesema mkutano huo umekuwa wa manufaa kwa Bara la Afrika na Ufaransa kwa pamoja kwani majadiliano yamegusa namna ya kuzifanya pande hizo mbili ziweze kunufaika na ushirikiano huo.
 
Amesema rasilimali zinazopatikana barani Afrika zinatosheleza ikiwa zitatumika vizuri katika kujenga uchumi wa Afrika.
 
“Lengo kubwa la jitihada hizi ni kupambana na umasikini lakini pia na kutengeneza ajira kwa makundi makubwa ikiwemo la vijana pamoja na wanawake,” amesema.
 
Aidha, Waziri Mkuu amesema maeneo mengi yaliyojadiliwa ni maeneo ambayo yamepewa umuhimu katika Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050.
 
“Nguzo zote zilizoongelewa kwenye dira lakini pia na maeneo ya kipaumbele yameguswa katika mijadala ya leo,” amesema.
 
Akizungumza katika mkutano huo, Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mheshimiwa Dkt. William Samoei Ruto, alizitaka nchi za Afrika kutafakari upya mifumo ya kiuchumi kwa kuimarisha ukusanyaji wa rasilimali za ndani, uwekezaji pamoja na ushirikiano wa kikanda ili kuhakikisha kunakuwa na maendeleo ya muda mrefu.
 
Aidha, Rais Ruto amesema ni wakati wa Afrika kujiweka kama mdau katika uchumi wa kimataifa badala ya kuwa mnufaika wa misaada ya nje pekee.
 
“Afrika haiwezi tena kubaki kama mshiriki asiyekuwa na sauti katika mifumo ya kimataifa ambapo baadhi ya maamuzi muhimu hufanywa bila sauti ya usawa,” alisema.
 
Kwa upande wake, Rais wa Jamhuri ya Ufaransa, Mheshimiwa Emmanuel Macron, alisema Bara la Afrika linapiga hatua kubwa za maendeleo na ni bara ambalo halisubiri majawabu ya changamoto bali linatoa majawabu ya changamoto mbalimbali lilazokabiliana nazo.

Katika hatua nyingine, Rais Macron alitangaza uwekezaji wa thamani ya dola za Marekani bilioni 27 barani Afrika katika sekta za nishati, Akili Unde, uchumi wa bahari pamoja na kilimo.
 
“Mpango huu utasaidia kutengeneza takriban ajira 250,000 barani Afrika na nchini Ufaransa,” alisema.
 
Aidha, Rais Macron aliwataka wafanyabiashara wa Afrika kuona fursa zilizopo nchini Ufaransa na kwenda kuwekeza.
 
“Hatuko hapa tu kuja kuwekeza katika Bara la Afrika pamoja nanyi, tunawahitaji viongozi wakubwa wa biashara wa Afrika kuja kuwekeza nchini Ufaransa,” alisema.
 
Kwa Upande wake Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres alisema watu wa Bara la Afrika wanapaswa kuwa wa kwanza kunufaika na rasilimali za bara hilo.
 
“Bara hili limebarikiwa rasilimali nyingi, hapa wenyewe ndio wanapaswa wawe wa kwanza kunufaika,” alisema.

Dkt. Mwigulu amemuwakilisha Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika mkutano.








Top News