Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Dodoma, Dkt. Neema Majule, amesema Bajeti ya Wizara ya Maji kwa mwaka wa fedha 2026/2027 inapaswa kuelekeza nguvu zaidi katika utafiti wa miamba na vyanzo vya maji ili kubaini maeneo yenye maji ya kutosha, kwa kuzingatia athari za mabadiliko ya tabia nchi.

Dkt. Majule ameyasema hayo Mei 6, 2026 bungeni Jijini Dodoma wakati akichangia Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Maji, ambapo alieleza kuwa pamoja na jitihada za serikali za kutoa maji kutoka kwenye mito na maziwa, ni muhimu kufanya tathmini ya mazingira ili kuhakikisha hatua hizo haziathiri viumbe hai na mfumo wa ikolojia.

Aidha, ameshauri serikali kuboresha na kukarabati miundombinu ya maji iliyochakaa ili kupunguza upotevu wa maji na kusaidia kufikia viwango vya kimataifa, Pia ameomba Wizara kutenga mfuko maalum wa matengenezo (Maintenance Fund) utakaowezesha ukarabati wa miundombinu kufanyika sambamba na udhibiti wa upotevu wa maji.

Katika mchango wake, Dkt. Majule amesema ndoto ya Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ya kupeleka maji kutoka Ziwa Victoria hadi Dodoma bado ina umuhimu mkubwa kwa maendeleo ya mkoa huo, amesema wananchi wa Dodoma wana matarajio makubwa kuona mpango huo unatekelezwa chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan na Waziri wa Maji, Jumaa Aweso, ili kuhakikisha huduma ya maji inawafikia wananchi kwa vitendo na si kubaki kwenye mipango ya maandishi pekee yaani makaratasi.





Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Prof. Riziki Shemdoe, amewapongeza walimu wa Mkoa wa Dodoma kwa jitihada zao zilizochangia kuongezeka kwa ufaulu katika ngazi zote za elimu kuanzia msingi hadi sekondari.

Akizungumza jijini Dodoma katika mkutano wa wadau wa elimu uliofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete Mei 6, 2026, Prof. Shemdoe amesema takwimu zinaonyesha mafanikio makubwa ya ufaulu kwa mwaka 2025 ikilinganishwa na mwaka 2024.

Ameeleza kuwa ufaulu wa darasa la nne uliongezeka kutoka asilimia 94.6 mwaka 2024 hadi asilimia 95.9 mwaka 2025, huku darasa la saba ukipanda kutoka asilimia 87.8 hadi asilimia 93.2. Kwa upande wa kidato cha pili, ufaulu uliongezeka kutoka asilimia 86.12 hadi 88.9, kidato cha nne kutoka asilimia 92.8 hadi 94.4, na kidato cha sita kutoka asilimia 99.86 hadi asilimia 99.87.

Amesema mafanikio hayo yanatokana na ushirikiano mzuri kati ya walimu, wanafunzi, viongozi na wadau wa elimu, akibainisha kuwa kaulimbiu ya mkoa huo kwenye sekta ya elimu isemayo “Uwajibikaji wangu ni msingi wa kuinua ubora wa elimu Dodoma” imechangia kwa kiasi kikubwa kutoa hamasa.

Prof. Shemdoe amesisitiza umuhimu wa kuongeza uwajibikaji katika sekta ya elimu kwa kusimamia taaluma, kudhibiti utoro wa walimu na wanafunzi, pamoja na kuhakikisha miradi ya ujenzi wa madarasa, shule mpya na vyoo inakamilika kwa wakati.

Aidha, amewataka viongozi kuhakikisha fedha zinazotolewa kwa ajili ya miradi ya elimu zinatumika kama zilivyokusudiwa, huku akihimiza ubunifu na bidii kazini ili kuongeza mafanikio zaidi.

Aidha Waziri Shemdoe amepinga vikali swala la ubaguzi kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum na kuwataka walimu kuhakikisha wanafunzi hao wanapata haki sawa ya elimu, pia amesisitiza umuhimu wa huduma ya chakula mashuleni, akiwataka wazazi kushiriki katika kuchangia chakula na Walimu kutumia maeneo ya shule kwa kilimo kwaajili yao na mengine kwaajili ya Wanafunzi ili kuhakikisha upatikanaji wa chakula cha uhakika.

Katika suala la nidhamu, Prof. Shemdoe amesisitiza kuwa adhabu kwa wanafunzi zinapaswa kutolewa kwa kuzingatia umri na kosa alilofanya mwanafunzi, sambamba na kufuata miongozo iliyopo badala ya maamuzi binafsi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, amesema mkoa huo umeendelea kunufaika na maboresho ya sekta ya elimu chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, ikiwemo ujenzi wa miundombinu na kuboreshwa kwa maslahi ya walimu.

Aliongeza kuwa mafanikio hayo yameiwezesha Dodoma kupanda kutoka nafasi ya kumi hadi nafasi ya pili kitaifa kwa ufaulu, huku lengo likiwa kushika nafasi ya kwanza.

Naye Katibu Tawala wa Mkoa wa Dodoma, Khatibu Kazungu, ameeleza kuwa mkutano huo umelenga kutathmini utekelezaji wa mpango mkakati wa elimu wa mwaka 2025, akibainisha kuwa utoaji wa tuzo kwa walimu umeendelea kuwa chachu ya kuongeza ari ya kazi na kuboresha matokeo ya wanafunzi kila mwaka.







Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Prof. Riziki Shemdoe, ametembelea banda la Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) wakati wa mkutano wa wadau wa elimu uliofanyika Mei 6, 2026 jijini Dodoma, ambapo alipata fursa ya kujionea shughuli mbalimbali zinazooneshwa na taasisi hiyo, kwa lengo la kufahamu mchango wao katika maendeleo ya sekta ya elimu.

Mkutano huo wa wadau wa elimu Mkoa wa Dodoma umefanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, ukiwa na kauli mbiu isemayo “Uwajibikaji wangu ni msingi wa kuinua ubora wa elimu Dodoma,” na mgeni rasmi alikuwa Waziri wa TAMISEMI, Prof. Riziki Shemdoe.









Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, akiwa kwenye picha na Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde, pamoja na Mwenyekiti wa Bodi ya Kampuni ya Perseus Mining Limited Bw. Rick Menell mara baada ya mazungumzo yao, Ikulu ya Chamwino, Dodoma tarehe 06 Mei, 2026.

Perseus Mining Limited ni mwekezaji wa Mgodi wa Dhahabu wa Nyanzaga, Wilayani Sengerema, Mkoani Mwanza kupitia Kampuni ya Sotta Minining Corporation Limited, inayomilikiwa kwa ubia na Serikali ya Tanzania.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde kwenye picha na Ujumbe wa Kampuni ya Perseus Mining Limited na Sotta Minining Corporation Limited mara baada ya mazungumzo yao, Ikulu ya Chamwino, Dodoma tarehe 6 Mei, 2026.

Perseus Mining Limited ni mwekezaji wa Mgodi wa Dhahabu wa Nyanzaga, Wilayani Sengerema, Mkoani Mwanza kupitia Kampuni ya Sotta Minining Corporation Limited, inayomilikiwa kwa ubia na Serikali ya Tanzania.








 

Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Serikali imetangaza kuwa ipo katika hatua za mwisho za kuandaa mfumo wa kisheria pamoja na sera maalum zitakazosimamia huduma za upandikizaji wa viungo, ikiwa ni jitihada za kurasimisha na kuimarisha sekta hiyo muhimu ya afya nchini.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kongamano la kimataifa la kisayansi lililoandaliwa na Hospitali ya Benjamin Mkapa lililolenga kujadili sera, mwelekeo na mikakati ya kuendeleza huduma za upandikizaji viungo, Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Grace Magembe, alisema maandalizi hayo yanatarajiwa kukamilika ifikapo Septemba mwaka huu.

Amesema  kuwa uwepo wa sera na sheria hizo utaweka misingi imara ya utoaji huduma hizo kwa kuzingatia viwango vya kitaifa na kimataifa, hali itakayosaidia kuongeza ufanisi na usalama kwa wagonjwa.

Dkt. Magembe alibainisha kuwa Tanzania imepiga hatua kubwa katika utoaji wa huduma za kibingwa na ubingwa bobezi, jambo linalowezesha wagonjwa wengi kupata matibabu ya hali ya juu ndani ya nchi badala ya kusafiri nje ya mipaka.

Alitaja mafanikio hayo kuwa ni pamoja na huduma za upandikizaji wa uloto kwa wagonjwa wa saratani ya damu pamoja na upandikizaji wa figo, huku akieleza kuwa mipango inaendelea ya kuanzisha huduma za upandikizaji wa ini na moyo katika siku za usoni.

Pamoja na mafanikio hayo, Dkt. Magembe alisisitiza umuhimu wa wananchi kujiunga na mifumo ya bima ya afya, akieleza kuwa huduma za upandikizaji viungo zina gharama kubwa ambazo si rahisi kumudu bila bima.

Alifafanua kuwa gharama za upandikizaji wa uloto zinaweza kufikia shilingi milioni 75, huku upandikizaji wa figo ukigharimu takribani shilingi milioni 40, hali inayofanya uwepo wa bima kuwa nguzo muhimu kwa wananchi wengi.

Kwa mujibu wake, hadi sasa zaidi ya wagonjwa 147 wamefanikiwa kufanyiwa upandikizaji wa uloto na figo hapa nchini, hatua inayopunguza utegemezi wa matibabu nje ya nchi na kuokoa gharama kubwa za usafiri na matibabu.

Aidha, alibainisha kuwa wagonjwa wa figo wanaohitaji huduma ya kuchuja damu hulazimika kufanya hivyo mara kadhaa kwa wiki, jambo linaloambatana na gharama na changamoto kubwa za maisha, hivyo bima ya afya inaweza kuwa suluhisho muhimu kwao.

“Ni muhimu wananchi wakaona umuhimu wa bima ya afya kama wanavyochukulia bima ya magari, kwa sababu inasaidia kukabiliana na gharama kubwa za matibabu,” alisisitiza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Benjamini Mkapa, Profesa Abel Makubi, aliipongeza serikali kwa uwekezaji mkubwa katika sekta ya afya, akisema hatua hiyo imewezesha kuboreshwa kwa huduma za kibingwa nchini.

Ameeleza kuwa kongamano hilo limewakutanisha zaidi ya wataalamu 150 wa afya kutoka mataifa mbalimbali kwa lengo la kubadilishana uzoefu na kuimarisha ujuzi katika huduma za kisasa za matibabu.

Profesa Makubi aliongeza kuwa hospitali hiyo imejikita katika kuendeleza huduma za upandikizaji viungo na itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha huduma hizo zinapanuka zaidi.

Kwa upande wa wanufaika, baadhi ya wagonjwa waliopatiwa huduma hizo walieleza mafanikio yao, wakisema matibabu hayo yamebadilisha maisha yao kwa kiwango kikubwa.

Miongoni mwao ni Richard Masimba, aliyefanyiwa upandikizaji wa figo miezi sita iliyopita, ambaye alieleza shukrani zake kwa madaktari na serikali kwa kumpa nafasi ya kuendelea kuishi maisha ya kawaida.

Naye Nasra Gwota alisema kabla ya kupandikizwa uloto alikuwa akisumbuliwa mara kwa mara na kulazimika kukosa masomo, lakini kwa sasa anaendelea vizuri na kurejea katika shughuli zake za kila siku.








 

Mwamvua Mwinyi, Pwani Mei 6, 2026

WATU wawili wamefariki dunia na wengine 14 kujeruhiwa kufuatia mgogoro wa ardhi uliotokea katika eneo la Vikawe (Lupaso), Kata ya Pangani, Wilaya ya Kibaha mkoani Pwani.
Akizungumza Mei 6, 2026, ofisini kwake wakati wa mkutano na waandishi wa habari, Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Mkoa wa Pwani, ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa huo, Abubakar Kunenge amekiri kutokea tukio hilo la uvunjifu wa amani . 

Amesema watu wasiojulikana walifika katika eneo hilo wakidaiwa kuwa na lengo la kuwaondoa wakazi wanaodaiwa kuvamia ardhi inayomilikiwa kihalali, hali iliyosababisha vifo vya watu wawili . 

Kunenge alieleza kuwa majeruhi wote wanapatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Pwani (Tumbi), huku miili ya marehemu ikiwa imehifadhiwa katika hospitali hiyo.

Jeshi la Polisi mkoani humo linaendelea na uchunguzi ili kubaini chanzo cha tukio hilo, mmiliki halali wa eneo pamoja na waliowatuma watu hao kwenda kuwaondoa wakazi.

Vilevile, amewataka wananchi kujiepusha na kujichukulia sheria mkononi  na uvamizi wa maeneo yasiyo yao.

“Wamiliki wa ardhi wanapaswa kufuata taratibu za kisheria wanapokumbana na migogoro, ikiwemo kufikisha suala hilo katika mabaraza ya ardhi au mahakamani. 

Pia,wamiliki endapo kuna amri ya mahakama ya kubomoa nyumba, washirikishe vyombo vya dola badala ya kuchukua hatua binafsi,” amesisitiza Kunenge.

Kwa upande wake, mkazi wa Chato, Vikawe, Kidawa Hamidu, aliiomba Serikali ya Mkoa pamoja na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuingilia kati mgogoro huo ili haki ipatikane kwa pande zote.

Naye Mwenyekiti wa Vikawe Shule, Shaban Shaban, alisema mgogoro huo ulikuwepo muda mrefu na tayari vikao mbalimbali vilishafanyika kutafuta suluhu, lakini bado haijafahamika nani aliwatuma watu hao kwenda kuwaondoa wananchi.

"Coaster zilikuwa kama tano, wakiwemo watu zaidi ya 200 wakidai wametumwa kwenda kubomoa nyumba za watu waliovamia eneo hilo" 

Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Dharura kutoka Hospitali ya Rufaa ya Tumbi, Siaely Moshi, alithibitisha kupokea majeruhi hao sanjali na vifo vya watu wawili wanaume, akieleza kuwa majeruhi kumi wanaendelea kupatiwa matibabu na wengine wanaendelea vizuri. 




 

 


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Dkt. Evaline Wilbard Munisi kuwa Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi Ajira na Mahusiano) kwenye hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma, tarehe 06 Mei, 2026.
Viongozi mbalimbali wakiapa kiapo cha Maadili kwenye hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 06 Mei, 2026. Kutoka kulia ni; Ndugu Kheri Abdul Mahimbali Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), Balozi Ali Jabir Mwadini, Katibu wa Rais, Mhandisi Peter Phillip Mwasalyanda Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Dkt. Jabir Kuwe Bakari Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Mhe. Angela Charles Kizigha, Mshauri wa Rais, Masuala ya Jamii




Viongozi mbalimbali wakiwa kwenye hafla ya Uapisho wa Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi Ajira na Mahusiano) Mhe. Dkt. Evaline Wilbard Munisi, Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 06 Mei, 2026


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Viongozi mbalimbali mara baada ya kumuapisha Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi Ajira na Mahusiano) Mhe. Dkt. Evaline Wilbard Munisi, Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 06 Mei, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na Waziri Mkuu Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, Spika wa Bunge Mhe. Mussa Azzan Zungu, Katibu Mkuu Kiongozi Mhe. Balozi Dkt. Moses Kusiluka, Kamishna wa Maadili Mhe. Jaji Sivangilwa Mwangesi katika picha na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi Ajira na Mahusiano) Dkt. Evaline Wilbard Munisi, Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 06 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi Ajira na Mahusiano) Dkt. Evaline Wilbard Munisi, Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 06 Mei, 2026.

WANANCHI wa manispaa ya Moshi mkoani Kilimanjaro wamelalamikia gharama za nauli za bajaji zinazofanya ruti zake kama daladala ndani ya manispaa hiyo na kuiomba Serikali kuingilia kati kunusuru adha hiyo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wananchi hao wamedai kuwa hapo awali walikuwa wakitozwa nauli ya 700 lakini kwa sasa wanatozwa 1,000- 1500 hali ambayo imegeuka kuwa adha kwao na kuwafanya wengi kushindwa kumudu gharama

Mmoja wa wananchi hao, Amina Salimu mkazi wa Soweto amesema kuwa, kwa sasa wamekuwa wakilazimika kutembea kwa miguu kutoka mjini Moshi kwenda na kurudi Soweto kutokana na kushindwa kuimili gharama za nauli.

"Mwanzoni tulikuwa tunatumia 1400 kwenda na kurudi Soweto lakini kwa sasa imeongezeka mpaka kufikia 2,000 hadi 3000 hii ni gharama ya kutuumiza sisi wananchi tunaiomba serikali kuingilia kati kutunusuru wananchi" alisema Amina.

Naye Rukia Juma ambaye ni mama lishe na mkazi wa Msaranga alisema kuwa kwa sasa ameanza kushindwa kumudu gharama za kuendesha familia kwani amekuwa akilipwa 4000 kwa siku lakini analazimika kutumia 3000 kwa ajili ya nauli hali ambayo imelekea kushindwa kumudu kutunza familia.

Mwananchi mwingine, Christofa Lyimo alisema kuwa, kwa sasa wamekuwa wakishindwa kwenda hospitali ya KCMC kuwaangalia na kuwahudumia wagonjwa wao ambao wamelazwa katika hospitali hiyo kutokana na gharama za usafiri kupanda.

Akijibu malalamiko hayo, Meneja wa mamlaka ya uthibiti wa usafiri ardhini (LATRA)mkoa wa Kilimanjaro, Paul Nyello alisema kuwa, Sheria ya LATRA haifanyi udhibiti wa tozo za bajaji na ni makubaliano ya abiria na mtoa huduma.

Alisema kuwa kwa sasa wapo katika mchakato wa kuongeza mabasi njia za mjini.


 



Na: Jawadu Kinyobwa – Arusha

Serikali imeagiza waajiri na wasimamizi wa rasilimaliwatu nchini kuhakikisha watumishi wote wenye sifa na waliotengewa bajeti ya kupandishwa Vvyeo Mei mwaka huu wanapandishwa vyeo bila kuwapo kwa ucheleweshaji wowote. 

Agizo hilo linasisitiza kukamilika kwa taratibu zote za kisheria na kanuni kwa wakati, huku Serikali ikionya kuwa haitavumilia malalamiko ya watumishi ambao haki zao zinakwama kutokana na uzembe wa maafisa utawala.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete, ametoa msimamo huo wakati akifungua mkutano wa pili wa Jumuiya za Wataalamu wa Utawala na Rasilimaliwatu (AAPAM Tawi la Tanzania) jijini Arusha Mei 06, 2026.

 Amebainisha kuwa Ofisi yake haitegemei kupokea malalamiko ya watumishi walioachwa wenye sifa huku akisisitiza kuwa watumishi waliojiendeleza lazima wabadilishiwe kada kulingana na miongozo iliyowekwa, kwani kufanya kinyume ni kutowajibika ipasavyo.

Waziri Kikwete ameeleza kuwa mageuzi ya utumishi wa umma yanategemea kwa kiasi kikubwa mchango wa wataalamu hao wa utawala na rasilimaliwatu.

Katika hatua nyingine, Waziri Kikwete ameagiza mabadiliko makubwa ya utendaji kazi ndani ya utumishi wa umma, akisisitiza kuwa kuanzia sasa maafisa rasilimaliwatu na utawala nchini lazima wahakikishe wanajenga usalama wa kisaikolojia kwa watumishi. 

Aidha Waziri amebainisha kuwa viongozi hao wana wajibu wa kutengeneza mazingira yanayofikika ili watumishi waweze kueleza changamoto zao bila hofu, hatua itakayosaidia kuepuka msongo wa mawazo na kuimarisha afya ya akili maeneo ya kazi.

Katika msisitizo wa matumizi ya teknolojia, Waziri ameelekeza matumizi kamili ya mifumo ya kielektroniki ikiwemo e-uhamisho, ambapo amepiga marufuku matumizi ya barua za kawaida katika mchakato wa uhamisho wa watumishi. 
Waziri amesisitiza pia umuhimu wa kuzingatia mwongozo wa kujitolea katika utumishi wa umma wa mwaka 2025, akitaka fursa za vijana kutolewa kwa njia ya uwazi na haki bila upendeleo wowote.

 Aidha, amewataka maafisa hao kuwa viongozi wa mageuzi katika taasisi zao kwa kupunguza urasimu na kushughulikia kero za watumishi katika ngazi ya taasisi badala ya kuziacha kuwa mzigo kwa mamlaka za juu. wananchi.

Vilevile, amewaagiza wataalamu hao kuhakikisha wanazingatia uadilifu na uzalendo kwa kuepuka matumizi ya lugha zisizofaa wanapowahudumia wateja wao, jambo ambalo linaharibu taswira ya serikali. 

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo, Xavier Daudi, amesema serikali imefanya maboresho ya muundo wa maofisa rasilimali watu tangu Septemba mwaka jana, ikiwa ni pamoja na kuhuisha mitaala na kuanzisha bodi ya kitaaluma kwa maofisa hao ili kuimarisha maadili na utendaji wao.

Naye Mwenyekiti wa AAPAM tawi la Tanzania, Leila Mavika, amesema zaidi ya washiriki 1,300 wamehudhuria mkutano huo, akibainisha kuwa unatoa fursa ya kubadilishana uzoefu na kujadili changamoto za kiutendaji katika sekta ya rasilimali watu.

Kwa upande wake, Rais wa AAPAM Afrika, Dk,John Nakabago, alisisitiza umuhimu wa serikali kuwekeza katika miundombinu ya kidijitali na kuhakikisha upatikanaji wa teknolojia kwa wote ili kufanikisha mageuzi ya kidijitali

Aliongeza kuwa ni muhimu kuwajengea uwezo watumishi wa umma, hususan walioko vijijini, ili waweze kutumia teknolojia ipasavyo. Pia alihimiza ushirikiano kati ya serikali, sekta binafsi, vyuo vikuu na asasi za kiraia katika kukabiliana na changamoto za ajira kwa vijana na mazingira.




 


Top News