ALBINISM Sports Club yenye Makao Makuu yake jijini Dar es Salaam kwa kushirikiana na Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TASACI), imeandaa mechi ya kirafiki kati ya timu ya Bunge.

Mechi hiyo ya kirafiki itakayofanyika Juni 6 2026 katika Uwanja wa Jamhuri, Jijini Dodoma na mtanange huo huo ni sehemu ya maandalizi kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Kuongeza Uelewa kuhusu Ualbino, ambayo huadhimishwa duniani kote Juni 13 Juni kila mwaka kwa lengo la kuhamasisha jamii kuhusu haki, usawa, heshima na ustawi wa watu wenye ualbino.

Taarifa iliyotolewa katika vyombo vya habari leo Juni 3,2026 na Abdallah Majiwa ambaye ni Mwenyekiti wa Albinism Sports Club amesema tukio hilo linatarajiwa kuwakutanisha pamoja Wabunge, watu wenye ualbino, wananchi wa Jiji la Dodoma na maeneo ya jirani na wadau mbalimbali wa masuala ya
haki za binadamu.

Amefafanua kuwa kaulimbiu ya mwaka huu ni: “Wezesha Watu Wenye Ualbino kwa Maendeleo Jumuishi na Endelevu.” Mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri wa Habari, Utamaduni,Sanaa na Michezo.

“Tunatoa mwito kwa wananchi wote wa Dodoma na maeneo ya jirani kujitokeza kwa wingi kushiriki na kuunga mkono tukio hili muhimu lenye lengo la kujenga jamii yenye usawa, heshima na fursa
kwa wote.

“Mbali na burudani ya michezo, mechi hii inalenga kuhamasisha ushirikishwaji wa watu wenye ualbino katika nyanja zote za maendeleo, kuongeza uelewa wa jamii kuhusu changamoto na fursa zinazowakabili, na kuendeleza mjadala kuhusu haki, usawa na fursa kwa watu wenye ualbino nchini Tanzania.”

Ameongeza malengo mahsusi ya mechi hiyo ni kuwaleta pamoja Wabunge, watu wenye ualbino na wadau mbalimbali ili kujenga mshikamano na kutafakari kwa pamoja namna bora ya kuwalinda, kuwawezesha na kuwaendeleza watu wenye ualbino;

Pia kuunganisha juhudi za Bunge, Serikali na wadau wengine katika kupinga unyanyapaa,kuondoa imani potofu, na kukomesha vitendo vya ubaguzi na ukatili dhidi ya watu wenye ualbino,kuelimisha jamii kuhusu masuala ya afya yanayowahusu watu wenye ualbino hususan umuhimu wa kinga dhidi ya miale ya jua na utunzaji wa afya ya ngozi;

Katika siku hiyo pia shughuli mbalimbali siku ya mechi ya waheshimiwa wabunge na watu wenye ualbino, inayotarajiwa kuanza saa 11 jioni na itatanguliwa na matukio mbalimbali muhimu yatakayolenga kuelimisha, kuhamasisha na kukuza ushirikishwaji wa watu wenye ualbino katika jamii.

Amesema matukio hayo ni pamoja na semina kubwa kuhusu masuala ya afya, mazingira na haki za watu wenye ualbino, utoaji wa huduma za afya ya ngozi, uwasilishaji wa risala ya waandaaji, hotuba fupi kutoka kwa viongozi mbalimbali wakiwemo waheshimiwa wabunge na mgeni rasmi pamoja na uzinduzi rasmi wa Albinism International Marathon.

Kuhusu Historia ya Siku ya Kimataifa ya Kuongeza Uelewa Juu ya Ualbino (13 Juni)
inatokana na Azimio la umoja wa mataifa kuhusu kuanzishwa kwa Siku ya Kimataifa ya Kuongeza Uelewa kuhusu Ualbino (International Albinism Awareness Day) lilipitishwa Desemba 18 2014 kupitia Azimio Na. A/RES/69/170 la Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa

Aidha Juni 13 ilichaguliwa kuwa siku rasmi ya maadhimisho hayo kwa sababu ndio tarehe ambayo Umoja wa Mataifa ulipitisha Azimio lake la kwanza kuhusu haki za watu wenye ualbino mwaka 2013.

Kuhusu Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira amesema ni mdau muhimu katika maadhimisho haya kupitia shughuli mbalimbali za elimu, afya na uhifadhi wa mazingira.

Mchango wake unajumuisha kuelimisha jamii kuhusu afya ya ngozi, kinga dhidi ya madhara ya mionzi ya jua kwa watu wenye ualbino, pamoja na kupinga imani potofu zinazochochea unyanyapaa na ukatili.Pia kukuza matumizi sahihi na salama ya tiba asilia kwa mujibu wa Sheria Na. 23 ya mwaka 2002 ya Tiba Asili na Tiba Mbadala.

Pia kuhamasisha utunzaji na uhifadhi wa mazingira kama msingi wa afya bora ya jamii,kulinda mimea tiba na rasilimali nyingine za asili kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho na kushirikiana katika kampeni za kupinga unyanyapaa, ubaguzi na ukatili dhidi ya watu wenye ualbino na watu wenye ulemavu kwa ujumla kupitia michezo na shughuli za kijamii.




Na Oscar Assenga, Tanga


Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Hamisi Mwinjuma (MB), amesisitiza umuhimu wa taasisi za kifedha nchini kuendelea kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya jamii kwa kuanzisha na kuunga mkono mipango inayolenga kuboresha maisha ya wananchi.

Akizungumza jijini Tanga wakati wa uzinduzi rasmi wa ushirikiano kati ya Bodi ya Mikopo kwa Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) na Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ) kupitia mpango wa “Cash Waqf”, Mwinjuma alisema ushirikiano huo ni hatua muhimu katika kuongeza upatikanaji wa rasilimali fedha za kufadhili elimu ya juu nchini.



Uzinduzi huo pia uliambatana na ufunguzi rasmi wa tawi la PBZ IKHLAS, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa benki hiyo wa kusogeza huduma za kifedha karibu zaidi na wananchi.

“Ni muhimu taasisi za fedha nchini kuendelea kushiriki katika maendeleo ya jamii kwa kuunga mkono mipango itakayowanufaisha wananchi katika maeneo mbalimbali,” alisema Mwinjuma.



Aidha, aliipongeza PBZ kwa juhudi zake za kupanua huduma za kifedha katika maeneo tofauti nchini, akibainisha kuwa hatua hiyo inachangia kuongeza ujumuishaji wa kifedha na kukuza uchumi wa taifa.

Pia aliwataka wananchi wa Mkoa wa Tanga kutumia kikamilifu fursa zinazotolewa na benki hiyo, ikiwemo huduma za akaunti, uwekezaji na mikopo, ili kuimarisha shughuli zao za kiuchumi na kuboresha ustawi wa maisha yao.



Kwa upande wake, Mkurugenzi Mwendeshaji wa PBZ, CPA Fahad Hamid, alisema benki hiyo iliyoanzishwa Juni 30, 1966, inakaribia kutimiza miaka 60 ya kutoa huduma za kifedha kwa wananchi wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.

Alisema PBZ inaendelea kupanua wigo wa huduma zake nchini, ambapo kwa sasa imefanikiwa kufika katika mikoa minane ya Tanzania Bara, hatua inayolenga kuwafikia wananchi wengi zaidi.



Naye Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB, Dkt. Bill Kiwia, alisema ushirikiano huo una lengo la kupanua vyanzo vya rasilimali fedha ili kuwawezesha vijana wengi zaidi kupata ufadhili wa masomo, hususan wanaojiunga na mafunzo ya amali kupitia vyuo vya kati.



Kwa mujibu wa Dkt. Kiwia, makubaliano hayo yataongeza uwezo wa HESLB kuwafikia wanafunzi wengi zaidi na kusaidia kuzalisha nguvu kazi yenye ujuzi unaohitajika katika viwanda na sekta nyingine za uzalishaji.



Akifafanua kuhusu mpango wa “Cash Waqf”, Meneja wa Uzingatiaji wa Shariah wa PBZ IKHLAS, Dkt. Issa Mohamed, alisema mpango huo unatoa fursa kwa watu binafsi, taasisi, wahisani na wawekezaji kuchangia au kuwekeza fedha zitakazosaidia kuongeza upatikanaji wa ufadhili wa elimu ya juu kwa vijana wa Kitanzania.



Alisema kupitia ushirikiano huo, PBZ na HESLB wanatarajia kuweka mfumo endelevu wa ukusanyaji na uwekezaji wa fedha kupitia mpango wa “Cash Waqf”, hatua itakayoongeza upatikanaji wa mikopo ya elimu ya juu na kuwawezesha wanafunzi wengi zaidi kutimiza ndoto zao za elimu.

Ushirikiano huo unatajwa kuwa miongoni mwa mikakati muhimu ya kuongeza fursa za elimu kwa vijana na kuchangia maendeleo ya rasilimali watu nchini.


-Pia imetuma ujumbe mzito kwa Bara la Afrika na dunia kwa ujumla


Na Said Mwishehe,Michuzi TV

ZIARA ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, nchini Urusi imeibua mjadala mkubwa ndani na nje ya mipaka ya Tanzania.

Wakati dunia ikiendelea kushuhudia mabadiliko makubwa ya kisiasa, kiuchumi na kidiplomasia, hatua ya Tanzania kuimarisha mahusiano yake na Urusi imeonekana kama ishara ya kujiamini, uhuru wa maamuzi na dira mpya ya diplomasia ya maendeleo.

Ziara hiyo, ambayo ni miongoni mwa ziara muhimu zaidi za ngazi ya juu kati ya Tanzania na Urusi katika miongo ya hivi karibuni, inajumuisha mazungumzo kati ya Rais Samia na Rais Vladimir Putin, ushiriki katika majukwaa ya biashara na uwekezaji pamoja na majadiliano yanayolenga kuimarisha ushirikiano katika elimu, sayansi, teknolojia, TEHAMA na sekta nyingine za kimkakati.

Diplomasia Isiyo na mipaka kwa mtazamo wa kidiplomasia, ziara hii inaakisi sera ya Tanzania ya kushirikiana na mataifa mbalimbali duniani bila kujifungamanisha na kambi moja ya kisiasa au kiuchumi.

Katika kipindi ambacho ushindani wa ushawishi kati ya mataifa makubwa duniani unaongezeka, Tanzania inaonyesha wazi kuwa iko tayari kufanya kazi na Mashariki, Magharibi na mataifa ya Kusini mwa Dunia kwa wakati mmoja, mradi ushirikiano huo unaleta manufaa kwa wananchi wake.

Hii ni ishara ya taifa linalojiamini katika maamuzi yake na linalotanguliza maslahi ya taifa kuliko siasa za makundi ya kimataifa. Kwa Afrika, hatua hii inaendana na mwelekeo wa nchi nyingi zinazotafuta washirika wengi wa maendeleo badala ya kutegemea upande mmoja.

 UCHUMI:JE,HAPA NDIPO FAIDA KUBWA ILIPO?

Kwa wengi, eneo la uchumi ndilo lenye matarajio makubwa zaidi kutokana na ziara hii.Ukweli ni kwamba lengo kuu ni kuongeza kiwango cha biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Urusi, huku matarajio yakielekezwa katika sekta za madini, nishati, elimu, teknolojia na miundombinu.

Iwapo makubaliano yatakayofikiwa yatawekwa katika vitendo, Tanzania inaweza kushuhudia ongezeko la uwekezaji wa moja kwa moja kutoka Urusi, upatikanaji wa teknolojia mpya, fursa za elimu kwa vijana na masoko mapya ya bidhaa za Tanzania.

Aidha, sekta ya utalii inaweza kunufaika kwa kuvutia wageni zaidi kutoka Urusi, jambo litakaloongeza mapato ya fedha za kigeni na kuchochea ukuaji wa biashara zinazotegemea utalii.

Hata hivyo, historia inaonyesha kuwa thamani ya makubaliano ya kimataifa hupimwa kwa utekelezaji wake, si kwa idadi ya nyaraka zinazotiwa saini. Mafanikio ya ziara hiyo yatategemea zaidi jinsi makubaliano hayo yatakavyotekelezwa katika miaka ijayo.

SIASA ZA KIMATAIFA NA SAUTI YA TANZANIA

Kisiasa, ziara hii inatuma ujumbe kwamba Tanzania inaendelea kujenga nafasi yake kama taifa lenye sauti huru katika medani ya kimataifa.

Kwa upande mmoja, hatua hiyo inaweza kuonekana kama juhudi za kuimarisha nafasi ya Tanzania ndani ya kundi la mataifa ya Global South na kupanua ushawishi wake katika masuala ya dunia.

Kwa upande mwingine, baadhi ya wachambuzi wa kimataifa wanaweza kuitafsiri kama ishara ya Tanzania kuimarisha zaidi mahusiano yake na Urusi katika kipindi ambacho Moscow inaendelea kuwa katika mvutano wa kisiasa na baadhi ya mataifa ya Magharibi.

Hata hivyo, sera ya Tanzania imekuwa wazi kwa miaka mingi: kujenga urafiki na kila taifa linaloheshimu maslahi ya Tanzania na kuchangia maendeleo yake.

Ushirikiano wa Kiusalama Wenye Fursa Mpya

Ingawa ajenda kuu ya ziara imejikita katika uchumi na biashara, ushirikiano wa kiusalama unaweza kuwa miongoni mwa maeneo yatakayonufaika kwa muda mrefu.

Maeneo yanayoweza kuimarishwa ni pamoja na mafunzo ya kijeshi, usalama wa mtandao, mapambano dhidi ya ugaidi, uhalifu wa kimataifa pamoja na kubadilishana uzoefu katika usimamizi wa mipaka na mifumo ya kiintelijensia.

Katika dunia inayokabiliwa na changamoto mpya za kiusalama, ushirikiano wa aina hii unaweza kusaidia Tanzania kuongeza uwezo wake wa kukabiliana na vitisho vinavyoibuka.

 ZIARA HII INATOA PICHA GANI KWA TANZANIA,AFRIKA NA DUNIA?

Kwa Tanzania, ziara hii inaonyesha taifa lenye utulivu wa kisiasa, sera huru ya mambo ya nje na uwezo wa kuvutia washirika wa kimataifa

Kwa Afrika, inatuma ujumbe kwamba bara hili halipaswi kutazamwa kama eneo la ushawishi wa upande mmoja, bali kama mshirika anayechagua mahusiano yake kwa kuzingatia maslahi ya maendeleo.

Kwa dunia, ziara hii ni ishara kwamba mfumo wa kimataifa unaendelea kubadilika kuelekea dunia yenye nguvu nyingi (multipolar world), ambapo mataifa ya kati kama Tanzania yanapata nafasi kubwa zaidi ya kujadiliana na kushirikiana na washirika mbalimbali kwa wakati mmoja.


 MANUFAA HALISI KWA TANZANIA NI YAPI?

Iwapo makubaliano yatatekelezwa kikamilifu, Tanzania inaweza kunufaika kupitia: Kuongezeka kwa uwekezaji na ajira. Kupanuka kwa biashara kati ya Tanzania na Urusi.

Fursa za elimu, utafiti na mafunzo kwa vijana. Uhamishaji wa teknolojia na maarifa ya kisasa. Kuongezeka kwa watalii na mapato ya fedha za kigeni. Kuimarika kwa nafasi ya Tanzania katika diplomasia ya kimataifa. Kupanuka kwa vyanzo vya ushirikiano wa maendeleo.

 Kwa mtazamo na tathmini yangu kwa jumla ni kwamba ziara ya Rais Samia Suluhu Hassan nchini Urusi ni zaidi ya ziara ya kawaida ya kidiplomasia. Ni hatua inayoweza kufungua milango mipya ya uchumi, uwekezaji, elimu, teknolojia na ushawishi wa Tanzania katika jukwaa la kimataifa.

Hata hivyo, mafanikio ya kweli hayatapimwa kwa picha za viongozi wakipeana mikono au makubaliano yanayosainiwa mbele ya kamera. Kipimo halisi kitakuwa ni kuona ndani ya miaka michache ijayo kama ziara hii itazalisha ajira, uwekezaji, biashara, teknolojia na maendeleo yanayogusa maisha ya Watanzania wa kawaida.

Ndipo historia itaamua kama safari ya Samia kwenda Moscow ilikuwa ziara ya kawaida au mwanzo wa ukurasa mpya wa maendeleo ya Tanzania.

ALICHOKISEMA RAIS SAMIA NCHINI URUSI 

Wakati mtazamo wako nikiweka katika maelezo  hayo ,Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kwa upande akiwa katika ziara hiyo anasema katika siku ya kwanza ya ziara yake ya kitaifa katika Shirikisho la Urusi pamoja na mambo mengine, amepata heshima ya kukutana na kufanya mazungumzo na Mheshimiwa Rais Vladimir Putin jijini Moscow.

Kwa mujibu wa Rais Samia amesema akizungumza katika mkutano wa waandishi wq habari baada ya kuzungumza na mwenyeji wake amesema ziara yake katika Shirikisho la Urusi ina umuhimu mkubwa wa kihistoria kwake binafsi na kwa taifa la Tanzania kwa ujumla.

Amesema imepita zaidi ya nusu karne tangu kufanyika kwa ziara ya mwisho ya kiserikali ya Tanzania nchini Urusi. Hivyo, kwake hiyo ni safari ya kihistoria sana kufika Urusi kujadili masuala mbalimbali ya ushirikiano wa pande mbili pamoja na maendeleo endelevu kwa wananchi wetu. 

Akasisitiza kwa niaba yake na wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ametoa shukrani za dhati kwa mwaliko huo.

Aidha amekumbusha mchango mkubwa wa Urusi katika harakati za Tanzania za kupigania uhuru na kumpongeza Rais Putin kwa maadhimisho ya miaka 81 ya ushindi katika Vita Kuu ya Pili ya Dunia yaliyofanyika Mei 9 mwaka huu.

Pamoja na hayo amesisitiza ziara hiyo inalenga kufungua fursa zaidi kwa wananchi na kuharakisha maendeleo ya kijamii na kiuchumi, wamejadili namna ya kuimarisha ushirikiano katika sekta mbalimbali za kimkakati, zikiwemo sayansi na teknolojia, elimu, nishati, madini, kilimo, miundombinu na utalii.

KAULI YA RAIS PUTIN MBELE YA RAIS SAMIA

Rais wa Urusi, Vladimir Putin, amesema taifa lake limekuwa likifuatilia kwa karibu mageuzi mbalimbali yanayofanyika nchini Tanzania na kuridhishwa na kasi ya maendeleo yake.

Amesema mazungumzo yake na Rais Samia yamekuwa yenye manufaa makubwa kwa mataifa yote mawili na kuahidi kuendelea kuimarisha ushirikiano kati ya Urusi na Tanzania katika sekta mbalimbali za maendeleo.


Simu 0713833822


Waziri wa Maji, Mhe. Jumaa Aweso (Mb), amefanya mabadiliko ya kimkakati katika katika Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) kwa kumteua Mhandisi Ndele Mengo kuongeza nguvu na kusimamia Idara ya uzalishaji na usambazaji maji DAWASA.

Mhandisi Mengo amepewa dhamana ya kusimamia uzalishaji na usambazaji maji kwa kuhakikisha huduma inaimarika na kukabiliana na changamoto za migao na upungufu wa maji Mkoan Dar ea Salaam na Pwani

Uteuzi huo ni ishara ya dhamira ya dhati ya Waziri Aweso ya kuhakikisha DAWASA inaongeza ufanisi kiutendaji na kufikia malengo ya Serikali ya kutoa huduma kikamilifu kwa Wananchi takribani Milion 7.2 wanaohudumiwa na Mamlaka hiyo.

Katika hatua nyingine, Waziri Aweso amemteua Mhandisi Christopher Gava kuwa Mkurugenzi wa Uwekezaji na Miradi DAWASA.

Akizungumzia mabadiliko hayo, Waziri Aweso amemtaka Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA, Mhandisi Mkama Bwire, kuendelea kusimamia utendaji kazi na kuchukua hatua kwa watendaji wababaifu watakaoshindwa kutatua changamoto za Wananchi na wasiokuwa na majibu ya utatuzi wa huduma.

“Nimefanya mabadiliko haya ili kuongeza nguvu DAWASA na kuhakikisha tunaimarisha eneo la uzalishaji na usambazaji Maji kwa ambayo ni kipaumbele cha msingi kwa Mwananchi”, amebainisha Mhe Aweso

Amesisitiza kuwa Mhandisi Mengo na timu yake wana jukumu la kuhakikisha uzalishaji unaendana na mahitaji na ratiba za upatikanaji wa Maji zinazingatiwa ili ilete maana halisi ya kumtua mama ndoo kichwani kwa vitendo.

Mhandisi Christopher Gava kuwa Mkurugenzi wa Uwekezaji na Miradi DAWASA.
 Mhandisi Ndele Mengo
Na Hafidh Kido


SAUTI kavu zenye mirindimo ya Kiafrika inasikika, lugha nzuri ya Kisambaa yenye sauti za kupanda na kushuka huku vishindo vya jembe la mkono vikinogesha sauti hizo.

Ni wakulima katika shamba la mahindi wakiimba huku wakiondoa magugu shambani, ni eneo ambalo miaka kadhaa iliyopita kulikuwa kukifanyika kilimo cha Mpunga. Kijiji cha Chekelei, Kata ya Chekelei, Tarafa ya Mombo Wilaya ya Korogwe mkoani Tanga.

Wakulima wanaelezea furaha yao kwa mwandishi wa Makala haya juu ya taarifa zinazowasaidia kujua wapande nini na mbegu za aina gani.

“Tunaishukuru serikali, inatuangalia kwa jicho la huruma. Tulikuwa tumeshakata tamaa juu ya mabadiliko haya ya hali ya hewa yasiyotabirika. Zamani hapa kulikuwa na maji yametuama, tulilila mpunga. Lakini baadaye maji yaliondoka, tulipata taarifa kwenye redio juu ya kubadili kilimo, tukaamua kuanza kulima mahindi,” anasema Amina Abdallah.

Aidha, wakulima hao wanaeleza wasiwasi wao juu ya athari za mabadiliko ya tabianchi yanayoathiri shughuli zao za kilimo. Lakini wanaamini tumaini bado lipo kutokana na kufikiwa na wataalamu mara kwa mara kuwapa taarifa sahihi.

Wanasema mvua hazitabiriki kama ilivyokuwa zamani, baadhi ya mazao yaliyokuwa yakistawi vizuri hayatoi mavuno ya kutosha, huku matumizi ya ardhi yakibadilika kutokana na mabadiliko ya upatikanaji wa maji.

Hata hivyo, wengi wao wanaeleza wana uelewa mdogo kuhusu mabadiliko ya tabianchi na namna ya kukabiliana nayo. Lakini tumaini lao lipo kwenye vyombo vya Habari.

Mzee Yusuph Kimea maarufu Mzee Mbega wa Kijiji cha Chekelei anaeleza kuwa eneo ambalo zamani lililimwa mkonge sasa linatumika kwa kilimo cha mpunga kutokana na kuongezeka kwa upatikanaji wa maji.

“Miaka ya nyuma hapa kulikuwa na mashamba ya mkonge ambao hustawi kwenye maeneo makame. Sasa tunalima mpunga unaohitaji maji mengi. Mahindi nayo hayafanyi vizuri tena kwa sababu mvua zimekuwa nyingi,” anasema na kuongeza:

“Hizi ni faida za taarifa tulizopata kupitia viongozi wetu wa Kijiji. Lakini zaidi kupitia kusikiliza redio hasa TBC. Lakini hapa tunayo pia redio yetu ya kijamii inaitwa Korogwe FM, vijana wale wanafanya kazi nzuri.”

Hata hivyo, Mzee Mbega anasema wakulima wanahitaji bwawa la umwagiliaji ili kupunguza utegemezi wa mvua ambazo hazina uhakika.


Mabadiliko ya tabianchi ni nini

Kwa mujibu wa Baraza la Kimataifa la Wataalamu wa Mabadiliko ya Tabianchi (IPCC), mabadiliko ya tabianchi ni mabadiliko ya muda mrefu ya hali ya hewa yanayosababishwa na michakato ya asili au shughuli za binadamu kama uchomaji wa mafuta ya kisukuku, kilimo na ukataji wa misitu. Mabadiliko haya huonekana baada ya miaka 30 au zaidi, si tukio la muda mfupi.

Shughuli hizi huzalisha gesi chafu kama dioksidi kaboni (CO₂), methani (CH₄) na nitrasi oksidi (N₂O) ambazo huchangia ongezeko la joto duniani. Athari zake ni pamoja na kuathiri uzalishaji wa chakula, upatikanaji wa maji, afya za watu na mifumo ya ikolojia.

Ingawa Tanzania huchangia kwa kiwango kidogo katika uzalishaji wa gesi chafu ukilinganisha na mataifa makubwa ya viwanda, ni miongoni mwa nchi zinazoathirika zaidi na mabadiliko ya tabianchi. Athari hizo zinaonekana katika sekta ya kilimo, usalama wa chakula, pamoja na maeneo ya pwani na kandokando ya maziwa makuu.

Umuhimu wa kuwaangalia wakulima wadogo unaonekana wazi katika takwimu za serikali. Utafiti wa Kilimo wa mwaka 2022/23 unaonyesha kuwa asilimia 95.4 ya ardhi inayolimwa nchini inategemea mvua, huku asilimia 85 ya wakulima wakiwa wakulima wadogo.

Kilimo kinaajiri zaidi ya asilimia 65 ya Watanzania na kuchangia zaidi ya robo ya pato la taifa. Hata hivyo, ni asilimia ndogo tu ya ardhi inayofaa kwa kilimo inayotumia umwagiliaji. Hali hii inaifanya sekta ya kilimo kuwa hatarini zaidi mbele ya mabadiliko ya tabianchi.

Katika juhudi za kukabiliana na changamoto hiyo, serikali imeendelea kuwekeza katika miradi ya umwagiliaji ili kupunguza utegemezi wa mvua na kuongeza uzalishaji wa mazao.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka Tume ya Taifa ya Umwaguiliaji (NIRC), Tanzania ina takribani hekta 694,715 zilizoendelezwa kwa umwagiliaji kufikia mwaka wa fedha 2024/25.

Serikali inatekeleza jumla ya miradi 780 ya umwagiliaji nchini, ikijumuisha skimu mpya, mabwawa na miundombinu mingine ya umwagiliaji. Lengo la taifa ni kufikisha eneo linalomwagiliwa hadi hekta milioni 1.2 ifikapo mwaka 2030.

Katika kuhakikisha miradi hiyo inafikiwa malengo yake, Serikali imeongeza bajeti ya maendeleo ya umwagiliaji kutoka shilingi bilioni 46.5 mwaka 2021/22 hadi shilingi bilioni 308.7 mwaka 2025/26.

NIRC pia imepewa mitambo yenye thamani ya Shilingi Bilioni 23.4 kwa ajili ya kuharakisha utekelezaji wa miradi ya umwagiliaji na uchimbaji wa visima.

Dunia inapigana vipi kukabili athari za mabadiliko ya tabianchi Kimataifa, juhudi za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi zimejikita katika maeneo makuu matatu.

Kwanza ni kupunguza uzalishaji wa gesi chafu ili kudhibiti ongezeko la joto duniani. Pili ni kujenga uwezo wa jamii kuhimili athari za mabadiliko ya tabianchi kupitia mbinu mbalimbali za kukabiliana nazo. Tatu ni kuhakikisha upatikanaji wa fedha za kusaidia nchi zinazoendelea kutekeleza mikakati ya kukabiliana na changamoto hizo.

IPCC inapendekeza matumizi ya mbegu zinazostahimili ukame, uhifadhi wa vyanzo vya maji, pamoja na mifumo ya tahadhari ya mapema ili kupunguza madhara yanayosababishwa na mabadiliko ya hali ya hewa.

Aidha, pamoja na juhudi zote zinazochukuliwa na mataifa mbalimbali duniani, wakulima hasa wadogo wanahitaji kupata taarifa sahihi na za kutosha kuhusu mabadiliko ya tabianchi.

Utafiti uliofanywa na mwandishi wa Makala haya katika vijiji vya Madumu na Chekelei wilayani Korogwe, umebaini kuwa redio ndiyo chanzo kikuu cha taarifa kwa wakulima wengi.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Madumu, Mohammed Rashid Kipimo, anasema ameanza kilimo tangu mwaka 1999 na ameshuhudia mabadiliko makubwa ya hali ya hewa. Lakini yeye na viongozi wenzie wamekuwa wakipata taarifa nyingi kupitia vyombo vya Habari.

“Miaka ya nyuma tulikuwa tunabadilisha mazao kulingana na mvua. Lakini mwaka 2008 tulikumbwa na jua kali na kupoteza mazao mengi, wakati huo wengi hatukujua chochote kuhusu athari za mabadiliko ya tabianchi,” anasema Kipimo.

Anasema maarifa yake kuhusu mabadiliko ya tabianchi yametokana zaidi na maafisa ugani wanaowashauri kutumia mbegu bora na mazao yanayokomaa kwa muda mfupi.

Kwa upande wake, Afisa Kilimo na Mifugo mstaafu, Richard Benard, anasema elimu inayotolewa kwa wakulima mara nyingi hujikita katika magonjwa ya mimea, wadudu waharibifu na pembejeo, huku masuala ya mabadiliko ya tabianchi yakipewa nafasi ndogo.

Anashauri wakulima kutumia redio na simu za mkononi kupata taarifa za hali ya hewa na ushauri wa kitaalamu unaoweza kuwasaidia kufanya maamuzi sahihi kuhusu kilimo.

Afisa Mazingira wa Wilaya ya Korogwe, Titus Onesmus, anasema changamoto kubwa si mwitiko wa wakulima kusikiliza redio, bali baadhi ya nyakati ni upatikanaji wa redio, lakini ofisi yake imekuwa ikiratibu vipindi vya redio kwa ajili ya kuwapa elimu wakulima na mwitiko ni mzuri.

Hata hivyo, anabainisha kuwa vyombo vingi vya habari binafsi hukabiliwa na changamoto za kifedha, jambo linalopunguza uwezo wao wa kuandaa vipindi maalumu vya mazingira bila ufadhili wa nje.

Mkurugenzi wa Korogwe FM, Dk. Adolph Noya, anakiri kuwa redio hiyo inakabiliwa na changamoto za rasilimali fedha na miundombinu, hali inayopunguza uwezo wa kufikisha taarifa za mazingira kwa wananchi wengi zaidi.

Anasema waandishi wa habari wanahitaji mafunzo zaidi kuhusu mazingira na mabadiliko ya tabianchi ili waweze kueleza masuala hayo kwa lugha rahisi inayoeleweka kwa wakulima.

Kutokana na hali hiyo, wadau mbalimbali wanapaswa kuimarisha matumizi ya redio za kijamii ambazo zina uwezo mkubwa wa kuwafikia wakulima kupitia lugha na mazingira wanayoelewa.

Serikali na wadau wa maendeleo wanashauriwa kufadhili mafunzo kwa wanahabari, kusaidia uzalishaji wa vipindi vya mazingira na kuboresha usikivu wa redio za kijamii.

Aidha, matumizi ya ujumbe mfupi wa simu (SMS), mifumo ya tahadhari ya mapema na vituo vya mawasiliano vya kijiji vinaweza kusaidia kuwafikishia wakulima taarifa muhimu kuhusu utabiri wa hali ya hewa, tahadhari za majanga na ushauri wa kilimo.

Kadiri mabadiliko ya tabianchi yanavyoendelea kuathiri uzalishaji wa chakula, umuhimu wa kuwapa wakulima wadogo taarifa sahihi, kwa wakati na zinazotekelezeka unaongezeka. Bila kufanya hivyo, kundi hili muhimu katika uchumi wa Tanzania litaendelea kubeba mzigo mkubwa wa athari za mabadiliko ya tabianchi.
Mwandishi wa makala haya akiwa kwenye shamba la mahindi la Mzee Mbega, anasema alidharau ushauri uliotolewa na wataalamu kutolima mahindi kwa sababu ya mvua kuwa nyingi.

Mwandishi wa makala haya akiwa na Mwenyekiti wa Kijiji cha Madumu, Mohammed Rashid Kipimo (mwenye fulana ya Blue) akimuonyesha maji ambayo yanatiririka kutoka milimani, ambapo wanakijiji wameshauri serikali ijenge bwawa litakalosaidia kulima mpunga mwaka mzima.


Na Karama Kenyunko Michuzi Tv
TANZANIA imepiga hatua kubwa katika mapambano dhidi ya usugu wa vimelea vya maradhi kwa dawa (AMR), kwa kupunguza matumizi holela ya dawa za antibiotiks kwa asilimia 88 na kupunguza vifo vinavyohusishwa na tatizo hilo kwa asilimia 14.

Hatua hiyp inatajwa kuwa mafanikio makubwa katika mapambano dhidi ya moja ya vitisho vikubwa vya afya vinavyoongezeka duniani.

Mafanikio hayo yametangazwaa leo Juni 3, 2026 Kongamano la 17 la Uwasilishaji wa Matokeo ya Tafiti za Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS), ambapo wataalamu walionya kuwa maambukizi yanayosababishwa na vimelea sugu kwa dawa bado ni tishio kubwa kwa afya ya umma, usalama wa chakula na ukuaji wa uchumi.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Uratibu wa Sekta Mbalimbali kuhusu Usugu wa Vimelea dhidi ya Dawa (MCC), Profesa Hezron Nonga, amesema mafanikio hayo yametokana na utekelezaji wa Mpango wa Pili wa Kitaifa wa Kukabiliana na AMR wa mwaka 2023–2028, unaotumia mkakati wa Afya Moja (One Health) unaounganisha afya ya binadamu, wanyama na mazingira.

"Tanzania imepiga hatua kubwa kutoka kuwa na uwezo mdogo wa kukabiliana na AMR mwaka 2016 hadi kuwa na mifumo imara ya kukabiliana na tatizo hilo kufikia mwaka 2024," amesema Profesa Nonga.

Ameeleza kuwa nchi imeimarisha mifumo ya ufuatiliaji wa magonjwa, kuboresha ushirikishanaji wa taarifa, kuongeza fedha za ndani kwa ajili ya shughuli za AMR na kuendesha kampeni za uhamasishaji wa umma kuhusu matumizi sahihi ya antibiotiki.

Hata hivyo, Profesa Nonga ameonya kuwa usugu wa vimelea dhidi ya dawa bado ni changamoto kubwa inayohitaji juhudi endelevu.

"AMR inaweza kufuta mafanikio yaliyopatikana katika sekta ya afya kwa miongo mingi. Ni muhimu kuendelea kuwekeza katika ufuatiliaji, tafiti na matumizi sahihi ya dawa za kuua vimelea ili kulinda ufanisi wa dawa zinazookoa maisha," amesema.

Duniani kote, AMR inahusishwa na takribani vifo milioni 4.71 kila mwaka, huku vifo milioni 1.14 vikisababishwa moja kwa moja na maambukizi ya bakteria sugu kwa dawa.

Tanzania pia imeongeza juhudi za kutoa elimu kwa umma kupitia kampeni ya "Holelaholela Itakukosti" pamoja na kuanzisha istilahi ya Kiswahili ya "Usugu wa Vimelea vya Magonjwa Dhidi ya Dawa (UVIDA)." Kampeni hiyo imewafikia karibu watu milioni 25 na kupata kutambuliwa na Kituo cha Afrika cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa (Africa CDC).

Kwa mujibu wa Profesa Nonga, utekelezaji wa hatua za kudhibiti maambukizi katika vituo vya afya umeongezeka kwa asilimia 60. Aidha, maboresho katika chanjo za mifugo, usalama wa kibaiolojia na usalama wa chakula yamechangia kupunguza milipuko ya magonjwa na matumizi yasiyo ya lazima ya dawa kwa wanyama.
Mkuu wa Ushirikiano wa Ubalozi wa Ufaransa nchini Tanzania, Luc Blanco, alisema usugu wa vimelea dhidi ya dawa ni miongoni mwa vitisho vikubwa vya afya duniani na akasisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa.

"Mapambano dhidi ya AMR yanahitaji ushirikiano wa sekta mbalimbali na nchi mbalimbali. Tafiti, ufuatiliaji na kubadilishana taarifa ni mambo muhimu kwa mafanikio ya juhudi hizi," amesema.
Makamu Mkuu wa Chuo cha MUHAS anayeshughulikia Mipango, Fedha na Utawala amesema vyuo vikuu vina nafasi muhimu katika kuzalisha ushahidi wa kisayansi unaosaidia kutunga sera na kuimarisha uwezo wa taifa wa kukabiliana na changamoto mpya za afya.

Kongamano hilo limewakutanisha watafiti, watunga sera, wataalamu wa afya na wadau wa maendeleo chini ya kaulimbiu: "Kuendeleza Mapambano dhidi ya AMR Tanzania: Taarifa za Mfumo wa Afya Moja kuhusu Mafanikio, Changamoto na Mwelekeo wa Baadaye."





Na Mwandishi wetu.
FILAMU ya uchunguzi iliyotengenezwa na mwanahabari wa uchunguzi kutoka Nigeria anayeishi Ghana, David Hundeyin, imeibua mjadala mpana kuhusu nafasi ya vijana, wajibu wa vyombo vya habari na umuhimu wa kulinda amani na utulivu katika jamii za Afrika.

Akizungumza baada ya kuonyeshwa kwa filamu hiyo, Waziri wa zamani wa Afya Zanzibar na mwanasiasa mkongwe,Hamad Rashid amesema kazi hiyo imefungua macho kwa wananchi kuhusu namna matukio makubwa ya kijamii na kisiasa yanavyoweza kuathiriwa na nguvu za nje, huku akisisitiza umuhimu wa Waafrika kujenga uwezo wao wa kufanya tafiti na uchunguzi wa kina kuhusu masuala yanayowahusu.

Amesema pamoja na filamu hiyo kutoa mafunzo muhimu kwa jamii, kinachopaswa kufanyika sasa ni kutumia yaliyobainishwa kama somo la kujenga taifa lenye amani, umoja na maendeleo badala ya kuendeleza migawanyiko. Alisisitiza kuwa changamoto kubwa zinazowakabili wananchi ni ajira, afya, elimu na ustawi wa maisha, hivyo nguvu kubwa inapaswa kuelekezwa katika kutatua mahitaji hayo.

Kwa upande wake, mwanazuoni na mchambuzi wa masuala ya maendeleo kutoka Zimbabwe, Joshua Maponga, alisema tukio hilo limeonesha umuhimu wa vyombo vya habari vya ndani kuwa na uwezo wa kuripoti kwa kina masuala yanayotokea katika jamii zao ili kutoa taswira halisi kabla simulizi za nje hazijatawala mjadala.

Ameongeza kuwa vijana wanapaswa kuwa waangalifu dhidi ya ushawishi unaoweza kuwaingiza katika migogoro inayoweza kuhatarisha mustakabali wao na maendeleo ya nchi zao kwani nguvu za vijana zinapaswa kuelekezwa katika ubunifu, uzalishaji na kujenga uchumi badala ya kushiriki katika matukio yanayoweza kuhatarisha amani.

Akielezea sababu za kuandaa filamu hiyo, David Hundeyin amesema lengo kuu lilikuwa kuonesha namna ambavyo ushawishi wa nje unaweza kujitokeza katika jamii za Afrika kupitia njia mbalimbali, ikiwemo mitandao ya kijamii na mashirika yenye maslahi ya kisiasa au kiuchumi.

Amesema Waafrika wengi bado hawatambui kwa kiwango kikubwa namna masuala ya kimataifa yanavyoweza kuathiri maisha yao ya kila siku, hivyo aliona umuhimu wa kutumia tukio hilo kama mfano wa kufundisha jamii kuhusu mazingira mapana ya kisiasa na kijamii yanayoikabili Afrika ya sasa.

Naye Mhariri Mkuu wa Wasafi Media, David Rweikiza Ronyagira, amesema filamu hiyo imewakumbusha wanahabari umuhimu wa kutafuta chanzo cha matukio badala ya kuripoti matokeo pekee kwani wanahabari wana wajibu wa kufanya tafiti za kina ili kusaidia jamii kuelewa sababu za changamoto mbalimbali na namna ya kuzitatua.

Aidha Ronyagira, filamu hiyo imeonesha kuwa kila mwananchi ana nafasi katika kulinda amani ya taifa, kuanzia viongozi, wanahabari, wanaharakati hadi wananchi wa kawaida. Alisema kila kundi linapaswa kutimiza wajibu wake kwa uwajibikaji ili kuzuia migogoro inayoweza kuepukika.

Akizungumzia vijana, amesema wanahitaji kupewa nafasi za kushiriki katika maendeleo ya taifa na kusikilizwa kuhusu changamoto zinazowakabili. Alionya dhidi ya tabia ya kutumia hasira za vijana kwa maslahi ya watu wengine badala ya kuwasaidia kupata suluhisho la matatizo yao.

Kwa upande wake, mwakilishi wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) Said salim, amesema pamoja na filamu hiyo kuwa mwanzo mzuri wa mjadala, bado ina maeneo yanayohitaji maboresho ya kitaaluma ili kutoa taswira pana zaidi ya matukio na athari zake kwa wananchi wa kawaida.

Washiriki wa mjadala huo walikubaliana kuwa somo kubwa lililotokana na filamu hiyo ni umuhimu wa kuimarisha elimu ya uraia, kuwajengea vijana uwezo wa kufanya maamuzi sahihi, kuimarisha uwajibikaji wa taasisi mbalimbali na kuhakikisha vyombo vya habari vinatimiza wajibu wake wa kuelimisha na kuhabarisha jamii kwa usahihi.

Wamesisitiza kuwa maendeleo ya taifa lolote hayawezi kupatikana bila amani, umoja na ushirikiano wa wananchi wake, huku wakitaka nguvu zaidi kuelekezwa katika kutatua changamoto za ajira, elimu na maisha bora kwa vijana ambao ndiyo nguvu kazi ya sasa na ya baadaye.




WAZAZI na wanafunzi nchini wamefurahishwa na maonesho ya vyuo vikuu Malaysia ambavyo vimewapa fursa mbalimbali za masomo nchini humo kwenye maonesho yaliyofanyika jana.

Akizungumza kwenye maonesho hayo, Mratibu wa maonesho, ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Elimu Vyuo Vikuu, Global Education Link (GEL), Abdulmalik Mollel, alisema maonesho yametoa fursa nyingi kwa vijana.

Mollel alisema vijana kutoka maeneo mbalimbali nchini wamefika kwenye maonesho hayo na kwamba kama kuna waliokosa nafasi wafike Global Education Link ambako watapatiwa fursa kama hiyo ya kuvijua vyuo hivyo.

“GEL inawahimiza wanafunzi, wazazi na walezi waliokosa kuhudhuria Maonesho ya Study in Malaysia katika Hoteli ya Serena kufika ofisi za GEL, ambako huduma za ushauri, udahili, scholarship na mwongozo wa kusoma Malaysia zinaendelea kutolewa kama ilivyokuwa kwenye maonesho,” alisema Mollel.

Mollel alisema maonesho hayo ya Study in Malaysia yamefungua fursa za Scholarship kwa wanafunzi wa Tanzania na kuongeza kuwa wazazi, walezi na wanafunzi waliohudhuria maonesho hayo Serena Hotel wameeleza kufurahishwa na fursa za scholarship, udahili wa moja kwa moja na mwongozo wa kusoma Malaysia.

Alisema Serikali imeeleza kuwa ujio huo unaunga mkono jitihada za kuimarisha elimu ya juu, kuongeza ushirikiano wa kimataifa na kuwajengea vijana uwezo wa kushindana duniani.

Aidha, alisema maonesho ya Study in Malaysia yamewakutanisha wanafunzi wa Tanzania na vyuo vikuu vinavyotambulika kimataifa kwa taaluma za afya, teknolojia, biashara, uhandisi na ubunifu.

Alisema kupitia maonesho hayo, wanafunzi wamepata taarifa za kozi, vigezo vya udahili, fursa za ufadhili na namna ya kujiandaa kwa elimu ya kimataifa.





Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma

Serikali imewataka Maafisa Utumishi na Wasimamizi wa Rasilimaliwatu nchini kutekeleza majukumu yao kwa weledi, uadilifu na kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za Utumishi wa Umma ili kuimarisha utoaji wa huduma na kupunguza malalamiko kutoka kwa watumishi pamoja na wananchi.

Wito huo umetolewa na Naibu Waziri wa Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Regina Qwaray, wakati akifunga kikao kazi cha Wakuu wa Idara na Vitengo vya Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu kutoka taasisi mbalimbali za Serikali.

Qwaray amesema Serikali inatarajia watumishi wa umma kusimamia haki za watumishi kwa mujibu wa sheria na kuhakikisha masuala yanayohusu maendeleo ya kiutumishi yanashughulikiwa kwa wakati. Amesisitiza kuwa malalamiko ya kutopandishwa madaraka, ucheleweshaji wa haki za watumishi na ukiukwaji wa maadili ya kazi yanapaswa kupatiwa ufumbuzi wa haraka ili kuimarisha mazingira bora ya utendaji kazi katika taasisi za umma.

Aidha, amewataka viongozi wa rasilimaliwatu kuhakikisha watumishi wanapatiwa mafunzo kuhusu usalama wa taarifa za Serikali na matumizi sahihi ya Akili Unde (AI) kwa kuzingatia maadili ya Utumishi wa Umma. Pia amesisitiza matumizi ya barua pepe rasmi za Serikali katika mawasiliano yote ya kikazi na kuonya kuwa hatua za kinidhamu zitachukuliwa dhidi ya watumishi watakaotumia vibaya mifumo hiyo au teknolojia ya Akili Unde kinyume cha taratibu zilizowekwa.

Katika hatua nyingine, Qwaray ameonyesha wasiwasi wake kuhusu dosari zinazojitokeza katika uendeshaji wa mashauri ya nidhamu, akisema baadhi ya waajiri wamekuwa hawafuati taratibu za kisheria hali inayosababisha watumishi waliotiwa hatiani kushinda rufaa zao. Amesema hali hiyo inaigharimu Serikali fedha nyingi na kuathiri taswira ya Utumishi wa Umma, hivyo amesisitiza umuhimu wa kuzingatia sheria na taratibu katika kushughulikia mashauri hayo.

Kuhusu utekelezaji wa Mfumo wa e-Utendaji, Naibu Waziri huyo amesema viongozi wa rasilimaliwatu wanapaswa kuhakikisha watumishi wanapatiwa mafunzo ya kutosha ili kuutumia mfumo huo kwa ufanisi. Amesikitishwa na taarifa za baadhi ya wasimamizi kushindwa kufanya tathmini za utendaji kazi kwa mwaka 2024/2025, jambo lililosababisha baadhi ya watumishi kunyimwa haki zao za maendeleo ya kiutumishi.

Kutokana na hali hiyo, amemuelekeza Katibu Mkuu (Utumishi) kwa kushirikiana na waajiri kuwabaini wasimamizi walioshindwa kutekeleza wajibu wao na kuwachukulia hatua kwa mujibu wa sheria. Pia amesisitiza kuwa watumishi walioathirika kutokana na uzembe wa wasimamizi wao wasikwamishwe katika maendeleo yao ya kiutumishi.

Hata hivyo Qwaray amewataka watumishi wote Nchini kukamilisha kwa wakati majukumu yao katika Mfumo wa e-Utendaji kabla ya Juni 30, 2026, huku akionya kuwa hatua kali zitachukuliwa dhidi ya viongozi na wasimamizi watakaoshindwa kutekeleza wajibu wao.





Na Mwandishi Wetu, Michuzi TV

TANZANIA na Malaysia zimefungua ukurasa mpya wa ushirikiano katika elimu ya juu kupitia ubia wa vyuo vikuu, tafiti za pamoja, ubadilishanaji wa wanafunzi na wahadhiri, ufadhili wa masomo pamoja na ushirikiano katika sayansi na teknolojia.

Vyuo Vikuu tisa vimeanza maonesho ya elimu katika Hoteli ya Serena kwa kutoa elimu na fursa ya watanzania kupata elimu katika nchi hiyo.

Akizungumza katika kikao cha Kuimarisha Ushirikiano wa Elimu ya Juu Kati ya Tanzania na Malaysia kilichofanyika Dar es Salaam, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Daniel Mushi amesema ujio wa ujumbe wa elimu kutoka Malaysia ni wa wakati muafaka wakati Tanzania ikiendelea kuimarisha na kutangaza kimataifa mfumo wake wa elimu ya juu.

Kikao hicho kiliandaliwa na kuratibiwa na Education Malaysia Global Services (EMGS) chini ya Wizara ya Elimu ya Juu ya Malaysia kwa kushirikiana na Global Education Link (GEL). Prof. Mushi amesema ujio wa ujumbe huo umevitambulisha vyuo vya Malaysia nchini Tanzania na kutoa nafasi kwa pande zote mbili kujadili maeneo ya ushirikiano yatakayowanufaisha wanafunzi, wahadhiri na taasisi za elimu ya juu.

Amesema Tanzania inatarajia kuona ushirikiano utakaoimarisha programu za pamoja, kubadilishana maarifa, tafiti, ubunifu na kuongeza uwezo wa taasisi za elimu ya juu nchini.

Aidha, amesema Malaysia imepiga hatua kubwa katika kutumia elimu, teknolojia na ujuzi kama nyenzo ya mageuzi ya kiuchumi, jambo ambalo Tanzania inaweza kujifunza katika safari yake ya kujenga uchumi unaotegemea maarifa na teknolojia.

Kwa mujibu wa Prof. Mushi, kipaumbele kinapaswa kuwekwa katika kuwaandaa wanafunzi wa Tanzania kwenye maeneo ya sayansi, hisabati, kemia, sayansi ya takwimu, ujifunzaji wa mashine na akili mnemba.

Amesema wanafunzi wanaotaka kusoma nje ya nchi wanapaswa kuandaliwa si kitaaluma pekee bali pia kilugha na kitamaduni ili waweze kushindana katika mazingira ya kimataifa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Elimu ya Juu katika Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Stephen Maluka amesema kikao hicho kimetoa jukwaa la vitendo kwa taasisi za Tanzania na Malaysia kujadili namna bora ya kujenga ushirikiano rasmi katika elimu, sayansi na teknolojia.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Global Education Link, Abdulmalik Mollel amesema GEL inajivunia kuratibu mpango huo unaounganisha taasisi za Tanzania na vyuo vikuu pamoja na mamlaka za elimu kutoka Malaysia. Amesema ushirikiano huo unalenga kujenga daraja la kweli kati ya Tanzania na Malaysia katika elimu ya juu kupitia tafiti, programu za kitaaluma, ubadilishanaji wa wanafunzi na wahadhiri pamoja na mafunzo yanayotegemea teknolojia.






Na Mwandishi wetu, DODOMA

Mkuu wa Kitengo cha Usafi na Udhibiti wa Taka Ngumu Jiji la Dodoma, Dickson Kimaro, amesema kuwa uwekaji wa vyombo vya kuhifadhia taka katika maeneo mbalimbali ya barabara ni sehemu ya mkakati wa kuimarisha usafi wa mazingira na kudhibiti utupaji holela wa taka ndani ya jiji hilo.

Akizungumza wakati wa zoezi la kuweka vyombo hivyo, Kimaro alisema kuwa hatua hiyo inalenga kuwahamasisha wananchi kutumia maeneo rasmi ya kutupia taka na kuongeza uwajibikaji katika utunzaji wa mazingira. Alibainisha kuwa uwepo wa vyombo vya kuhifadhia taka utarahisisha ukusanyaji wa taka na kuifanya Dodoma kuwa jiji safi, salama na lenye mazingira bora kwa wakazi na wageni.

"Tunawaomba wananchi watumie vihifadhi taka hivu kwa usahihi na kuepuka kutupa taka hovyo. Ushirikiano wa jamii ni muhimu katika kuhakikisha tunadumisha usafi wa jiji letu wakati wote. Tutaimarisha ulinzi kwenye hizi barabara ili kuhakikisha vyombo hivi haviharibiwi ukizingatia tumeweka kamera za ulinzi katika barabara zetu za jiji pia kwa yeyote atayekiuka agizo sheria zitafuatwa dhidi yake" alisema Kimaro.

Aidha, alieleza kuwa mamlaka za jiji zitaendelea kuboresha huduma za usafi wa mazingira kwa kuongeza miundombinu ya kuhifadhi taka pamoja na kuimarisha elimu kwa umma kuhusu umuhimu wa usafi na utunzaji wa mazingira.

Alisema vyombo hivyo si vyakuwekea taka kutoka majumbani bali ni kuwasaidia wanaopita barabani kutupa taka mfano chupa za maji na magunzi ya mahindi.

Zoezi hilo ni sehemu ya jitihada zinazoendelea za Jiji la Dodoma za kuboresha mazingira yake ili kuzuia uchafuzi wa mazingira na kulinda afya za wananchi.





Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita limemtia nguvuni Peter Willium (28), mkazi wa Kijiji cha Itale, Wilaya ya Chato kwa tuhuma za kumteka na kumbaka Mwanafunzi, ambaye utambulisho wake umehifadhiwa kwa mujibu wa sheria.

Kwa mujibu wa taarifa ya polisi, tukio hilo la kusikitisha lilitokea tarehe 31 Mei 2026, majira ya saa sita mchana. Eneo la tukio ni Pori la Ichwankima lililopo ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Burigi, Wilaya ya Chato.

Inadaiwa kuwa mtuhumiwa alimvamia mwathirika, akamkokota hadi vichakani na kumfanyia ukatili wa kingono. Baada ya kitendo hicho, hakumuachia huru mwathirika. Badala yake, aliwasiliana na familia ya msichana huyo kupitia simu, akiwataka wamtumie fedha ili amwachie. Aliongeza vitisho kuwa atamdhuru iwapo hawataitikia matakwa yake.

Baada ya kupata taarifa, polisi walifanya operesheni ya kimsako na kufanikiwa kumtia mbaroni mtuhumiwa. Kwa sasa mahojiano yanaendelea na upelelezi unakaribia kukamilika ili mtuhumiwa afikishwe mbele ya vyombo vya sheria.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita amewashukuru wananchi waliofanikisha kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo. Amehimiza jamii kuendelea kutoa taarifa za ukatili dhidi ya watoto na wanafunzi. Pia ameonya kuwa jeshi hilo litachukua haytua kali kwa mtu yeyote atakayethibitika kuhusika na uhalifu wa aina yoyote.




Top News