Na Mwandishi Wetu.

KAMPUNI ya Oryx Gas Tanzania kwa kushirikana na taasisi ya Kidoti Foundation wameingia makubaliano ya kuendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi nchini kwa kulifiki kundi la watoa huduma za Saluni nchini.

Kwa mujibu wa Oryx na Kidodi Foundation watoa huduma za Saluni nchini ni kundi lenye uwezo mkubwa wa kuharakisha matumizi ya nishati safi ya kupikia kutokana na mwingiliano wao wa karibu na jamii, hali inayowafanya kuwa mabalozi muhimu wa mabadiliko ya tabia na mtazamo kuhusu matumizi ya nishati hiyo.

Akizungumza Jijini Dar es Salaam wakakati wa hafla ya kusaini makubaliano hayo Mkurugenzi wa Kidoti Foundation, Jokate Mwegelo, ambaye pia ni mlezi wa Chama cha Salunisti Tanzania (CCST) amesema lengo la kuwawezesha watoa huduma za saluni kutumia nishati safi na kuwa mabalozi wa kuhamasisha matumizi yake katika jamii.

Amesema kundi la wasusi na watoa huduma za saluni lina nafasi ya kipekee kwa kuwa hukutana na mamia ya wananchi kila siku, jambo linaloweza kutumiwa kueneza elimu kuhusu manufaa ya nishati safi ya kupikia kwa urahisi kuliko kutegemea kampeni za kawaida pekee.

Amefafanua watoa huduma za saluni wanazungumza na watu wa makundi mbalimbali kila siku. Wanajenga mahusiano ya karibu na wateja wao, hivyo wana nafasi kubwa ya kubadilisha mitazamo kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia.

“Tunataka wawe mabalozi wa mabadiliko hayo na kupitia makubaliano haya tumeyaingia Kati ya Kidoti Foundation na Oryx Gas Tanzania matarajio yetu tutawafikia watoa huduma wote wa saluni kupitia chama chao ambapo tutawapatia mitungi ya gesi na tutaanza na mitungi 2000 ambayo itatolewa kwa awamu.

Juhudi za kuhakikisha Watanzania wengi wanatumia nishati safi haziwezi kuachiwa Serikali pekee, bali zinahitaji ushiriki wa makundi yenye ushawishi wa moja kwa moja katika jamii.

Kundi la watoa huduma za saluni limesahaulika kwa muda mrefu lakini Kidoti Foundation tumeona iko haja ya kulishika kundi hili kwa kuliwezesha kutumia nishati safi ya kupikia.”

Jokate amesema saluni zimekuwa sehemu ambazo mbali na huduma za urembo, wananchi hubadilishana uzoefu kuhusu afya, biashara, malezi na masuala mbalimbali ya maendeleo, hivyo zinaweza pia kuwa majukwaa ya utoaji wa elimu kuhusu nishati safi.

Pia amesema kupitia ushirikiano huo, watoa huduma za saluni watanufaika kwa kutumia nishati safi katika shughuli zao za kila siku, huku wakipata nafasi ya kuwahamasisha wateja wao kuachana na matumizi ya nishati zinazochafua mazingira na kuhatarisha afya.

"Nishati safi si suala la kupikia pekee. Ni suala la afya, mazingira, uchumi wa familia na maendeleo ya taifa. Tukiwafikia wasusi, tutakuwa tumefikia maelfu ya familia kupitia wateja wao," amesema.

Kwa upande wake Meneja Mauzo wa Oryx Tanzania Shaban Fundi amesema kampuni hiyo imeamua kushirikiana na Kidoti Foundation kwa kutambua kuwa makundi ya kijamii yenye ushawishi yanaweza kuongeza kasi ya matumizi ya nishati safi nchini.

“Mbali na kutoa suluhisho la nishati safi, kampuni yetu itaendelea kujenga uelewa wa wananchi kuhusu faida za matumizi ya gesi na teknolojia nyingine za kisasa zinazochangia kulinda afya na mazingira,”amesema na kusisitiza Oryx Gas na Kidoti Foundation kupitia makubaliano yanakwenda kuongeza watumiaji wa nishati safi nchini.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CCST Ntuli Mwakatobe amesema amesema ushirikiano huo ni hatua muhimu ya kuwawezesha wanachama wa chama hicho kuwa sehemu ya utekelezaji wa ajenda ya nishati safi nchini.

Amesema wasusi na wamiliki wa saluni wamekuwa wakitafuta njia za kupunguza gharama za uendeshaji wa biashara zao huku wakihakikisha mazingira ya kazi yanakuwa salama zaidi.

"Leo tunapata nafasi ya kutumia nishati safi lakini pia kuwa sauti ya kuelimisha jamii. Hii ni fursa ambayo tutaenda kuitumia kuwafikia wateja wetu kila siku," amesema.

Matumizi ya nishati safi ya kupikia yanatajwa kuchangia kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa unaochochea mabadiliko ya tabianchi, sambamba na kuboresha maisha ya wanawake ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakibeba mzigo mkubwa wa shughuli za kupikia.





Na Seif Mangwangi, Michuzi TV, Arusha


VIJANA zaidi ya 77, 000 kutoka mikoa nane wanaojishughulisha na ujasiriamali wa kilimo na ufugaji nchini, wamepatiwa mafunzo ya matumizi sahihi ya fedha Ili kuwasaidia kuboresha shughuli zao na jamii inayowazunguka.

Mafunzo hayo ambayo yametolewa na chuo cha Benki Kuu ya Tanzania (BOT), kwa ufadhili wa mfuko wa chakula Duniani (WFP), vijana hao wametoka katika mikoa ya Arusha, Manyara, Morogoro, Dodoma, Shinyanga, Simiyu, Tabora na Singida.

Akizungumza wakati wa kufunga mahafali ya kuhitimu mafunzo hayo kwa vijana kutoka mikoa mitano ya Morogoro, Arusha, Singida, Dodoma na Manyara , Mkuu wa chuo cha benki Kuu Tanzania, Dk.Nicas Yuna amesema elimu waliyopewa vijana hao ni silaha ya kuwakwamua kiuchumi.

Amesema vijana hao wanatakiwa kutumia elimu waliyoipata kupitia mafunzo hayo kuwafundisha vijana wengine na kwamba chuo cha benki kuu kitafuatilia kujua matokeo ya mafunzo hayo kwa Kila kijana aliyehudhuria.

“ Haya ni mafunzo ambayo yanatakiwa kusambaa zaidi, na hawa ni vijana wachache walioteuliwa Ili waweze kwenda kuwa walimu Kwa vijana wengine, tunaamini wakiisambaza elimu hii vizuri, vijana wengi watafaidika na kujikwamua kiuchumi,” amesema Dkt Yuna.

Amesema katika mafunzo hayo ambapo pia walialikwa wakufunzi kutoka taasisi za benki ili kutoa elimu ya namna ya kukopa, bima kwaajili ya usalama wa mazao na mifugo pamoja na mfuko wa uwekezaji UTT, walifundishwa masomo ya namna ya kutafuta fedha halali, kubana na kutunza fedha kwaajili ya uwekezaji.

Afisa habari wa WFP nchini, Brigitha Lyimo amesema mafunzo hayo ni muendelezo wa mradi wa miaka mitano wa vijana kilimo Biashara kwaajili ya kuwawezesha vijana katika ujasiriamali wa kilimo ulioanza mwaka 2023.

Kaimu Mkurugenzi wa WFP nchini Tanzania, Christine Mendes amelishukuru shirika la Mastercard foundation Kwa ufadhili wa programu hiyo ya kumwezesha kijana na kusema ni matarajio ya WFP kuwa wahitimu wa mafunzo hayo wataenda kuibadilisha jamii wanayotoka kwa kuendeleza kilimo na ufugaji kwa kutumia mbinu za kisasa za matumizi sahihi ya fedha.

“ Kwa msaada wa mfuko wa wakfu wa Mastercard, WFP inatekeleza programu ya Vijana Kilimo Biashara (VKB), Ili kuunda na kutengeneza fursa za kazi zenye heshima na utiifu Kwa vijana kupitia mnyororo wa thamani ya kilimo,pia programu hii inatambua kuwa uwezo wa kifedha ni muhimu kwa ujasiriamali, ukuaji wa biashara na mabadiliko ya muda mrefu ya kiuchumi,” Amesema.

Amesema katika mahafali hayo ambapo jumla ya wahitimu walimu wa fedha 79 walihitimu na kukabidhiwa vyeti, kunakamilisha idadi ya wahitimu 150 kufuatia vijana wengine71 kuhitimu mafunzo ya aina hiyo hiyo Jijini Mwanza na kwamba Mtandao huo unaokua unawakilisha uwekezaji muhimu Kwa watu na taasisi ambao utaendelea kuimarisha ushirikishwaji wa fedha Tanzania nzima.

Amesema mafunzo hayo yatawasaidia vijana kukuza ujasiri wa kuweka akiba, kuwekeza, kuweka rekodi, kupata huduma za kifedha na kufanya maamizi sahihi ya kibiashara.








Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB), Bw. Asangye Bangu, amesema Bodi inatarajia kuongeza bidhaa nyingine tano katika Mfumo wa Stakabadhi za Ghala ili kuendelea kuwanufaisha watanzania katika sekta mbalimbali.

Akifungua kikao cha wadau cha kujadili na kupitisha Rasimu ya Mpango Mkakati wa WRRB wa miaka mitano (2026/27–2030/31) pamoja na kupokea maoni kuhusu maboresho ya Kanuni za Stakabadhi za Ghala, kilichofanyika Juni 26, 2026, mjini Morogoro, Bw. Bangu amesema mfumo huo umeendelea kukua kwa kasi na kuleta mafanikio makubwa.

Amesema katika kipindi cha miaka mitano iliyopita mfumo huo ulikuwa unahusisha bidhaa mbili pekee, lakini kwa sasa unahusisha bidhaa 18, huku maandalizi yakiendelea kuongeza bidhaa nyingine tano ili kuimarisha uwazi, ushindani wa bei na kuongeza fursa za biashara ya mazao.

Bw. Bangu amebainisha kuwa pamoja na kuwanufaisha wakulima kwa kuwawezesha kuuza mazao yao kwa bei yenye ushindani, mfumo huo umechangia kuongeza mapato ya Serikali na kurahisisha Halmashauri kukusanya mapato yatokanayo na biashara ya mazao.

Aidha, amesema WRRB inaendelea na mazungumzo na Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) pamoja na Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko (CPB) ili kuwezesha biashara ya mazao kufanyika kupitia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala, hatua itakayoongeza ufanisi na uwazi katika biashara hiyo.

Ameongeza kuwa Bodi itaendelea kuhamasisha matumizi ya mfumo huo kwa kuanzisha njia bunifu zitakazowasaidia wakulima kuepuka kuuza mazao yao mara tu baada ya mavuno, wakati bei zikiwa chini.

Benki ya NMB na Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Maendeleo ya Mitaji (UNCDF) wamesaini Hati ya Ushirikiano inayolenga kuimarisha mazingira ya kuibua, kukuza na kupanua kampuni changa zenye mawazo bunifu ya kidijitali kupitia uwezeshaji wa kisera na kisheria, masoko, mitaji na ushauri wa kitaalamu.

Makubaliano hayo yamesainiwa jijini Dar es Salaam na Afisa Mkuu wa Teknolojia na Mabadiliko ya Kidijitali wa Benki ya NMB, Kwame Makundi, pamoja na Katibu Mtendaji wa UNCDF, Pradeep Kurukulasuriya. Ushirikiano huo unaendeleza Programu ya PesaTech, iliyoanzishwa mwaka 2022 na ambayo tayari imeziwezesha kampuni changa 22 za teknolojia ya fedha.

Makundi alisema kampuni tano tayari zinafanya kazi na NMB, huku tatu zikiunganisha huduma zake katika NMB Mkononi Super App. Benki hiyo inalenga kuingiza zaidi ya kampuni changa 30 katika mfumo wake ifikapo mwaka 2030 na kuziunganisha na mitaji, masoko, wataalamu na mifumo ya kidijitali.

Kurukulasuriya alisema UNCDF inaiona NMB kuwa mshirika muhimu katika kukuza kampuni changa na kuyageuza mawazo bunifu kuwa biashara zenye uwezo wa kuongeza ajira na kutatua changamoto za wananchi
Afisa Mkuu wa Teknolojia na Mabadiliko ya Kidijitali wa Benki ya NMB, Kwame Makundi (katikati), akibadilishana Hati ya Makubaliano iliyosainiwa na Katibu Mtendaji wa Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Maendeleo ya Mitaji (UNCDF), Pradeep Kurukulasuriya, jijini Dar es Salaam. Makubaliano hayo yanaendeleza awamu ya tatu ya Programu ya PesaTech, itakayowezesha kampuni za teknolojia ya fedha na kampuni changa kupata ushauri wa kitaalamu, masoko na fursa za kuunganisha suluhisho zao katika mfumo wa kidijitali wa NMB. Anayeshuhudia kushoto ni Mkuu wa Miundombinu na Ushirikiano wa Kikanda katika Ujumbe wa Umoja wa Ulaya nchini Tanzania na Jumuiya ya Afrika Mashariki, Paola Trevisani.



Afisa Mkuu wa Teknolojia na Mabadiliko ya Kidijitali wa Benki ya NMB, Kwame Makundi (aliyeketi kushoto), na Katibu Mtendaji wa Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Maendeleo ya Mitaji (UNCDF), Pradeep Kurukulasuriya, wakisaini Hati ya Makubaliano jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kuendeleza awamu ya tatu ya Programu ya PesaTech, inayolenga kuimarisha mfumo wa kampuni za teknolojia ya fedha na kampuni changa za kibunifu nchini Tanzania. Anayeshuhudia katikati ni Mkuu wa Miundombinu na Ushirikiano wa Kikanda katika Ujumbe wa Umoja wa Ulaya nchini Tanzania na Jumuiya ya Afrika Mashariki, Paola Trevisani, akiwa na viongozi wengine.





















Top News