Veronica Simba - WMA 

Wakala wa Vipimo (WMA) umesimika mtambo wa kisasa wa kidijitali wa kuhakiki dira za maji katika jengo la makao yake makuu lililopo jijini Dodoma.

Meneja Uhakiki wa Vipimo na Viwango wa WMA Makao Makuu, Magesa Biyani amesema usimikaji mtambo huo uliogharimu takribani shilingi milioni 400, utawezesha uidhinishaji na uhakiki wa dira za maji kwa muda mfupi na kwa usahihi zaidi kupitia miradi mingi ya maji inayoendelea kutekelezwa nchini ikiwemo Mkoa wa Dodoma na mikoa mingine jirani.

Akizungumza na wanahabari wa WMA Februari 3, 2026, Biyani amesema kuwa “Mtambo huu umekuja kwa wakati mwafaka kuwezesha wafanyabiashara pamoja na Mamlaka za Maji kuzingatia kwamba dira za maji zote ambazo wanawafungia wateja katika maeneo yao ziwe zimehakikiwa na WMA ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma kulingana na thamani ya fedha wanazolipa.”

Akifafanua zaidi, amesema kuwa mtambo huo una uwezo wa kuhakiki dira za maji nyingi zaidi kwa wakati mmoja kwa kutumia muda mfupi zaidi tofauti na mitambo ya awali ambayo ni ya ki-makenikali (Mechanical Test Bench) yenye uwezo wa kuhakiki dira za maji 10 kwa wakati mmoja ikitumia dakika 20 hadi 30.

Amesema kuwa mtambo huo pamoja na mingine miwili ya aina hiyo iliyoko katika Kituo cha Uhakiki Vipimo, Misugusugu mkoani Pwani, kwa pamoja imeleta faida kubwa ikiwemo kupima dira za maji nyingi zaidi, kwa usahihi zaidi na kwa muda mfupi tofauti na awali kabla ya uwepo wake.

Akitoa mfano, Biyani amesema mathalani kwa Kituo cha Misugusugu ambako mitambo ya aina hiyo ilitangulia kusimikwa kabla ya Dodoma, dira za maji kati ya laki mbili hadi laki tatu zimekuwa zikipimwa kwa mwaka kutegemea na uhitaji kutokana na kuongezeka kwa miradi ya kimkakati.

“Kwahiyo imeleta faida kubwa sana na kusaidia thamani ya fedha iweze kuonekana kwa wateja/wananchi, Mamlaka za Maji na wafanyabiashara na hata kwa uchumi wa nchi,” ameeleza Biyani.

 Akidadavua zaidi namna WMA inavyohusika katika uidhinishaji na uhakiki wa dira za maji, ameeleza kuwa hilo ni mojawapo ya majukumu yake ya uhakiki wa vipimo vya aina mbalimbali nchini kwa lengo la kumlinda mlaji.

Amesema kuwa, WMA huidhinisha na kuhakiki vipimo kwa niaba ya Serikali ambapo kwa upande wa dira za maji, mfanyabiashara yeyote binafsi au kampuni kabla ya kuagiza au kuzalisha bidhaa hizo anatakiwa awasilishe sampuli yake WMA ili kuhakiki muundo wake na baada ya kuidhinishwa anatakiwa kuziwasilisha bidhaa zote alizoagiza au kuzalisha ili zihakikiwe kwa kila moja kujiridhisha kuhusu usahihi wake.

Biyani amefafanua zaidi kuwa zoezi hilo hulenga kuzilinda pande zote mbili yaani mteja na muuzaji ili yeyote kati yao asipunjwe. Dira za maji zilizohakikiwa humuwezesha mteja kulipia kiwango stahiki kulingana na matumizi yake ilhali kwa upande wa muuzaji humwezesha kupata malipo stahiki kulingana na huduma anayotoa.

Akijibu swali la mwandishi kuhusu mipango ya WMA kufikisha huduma hiyo nchi nzima, Biyani ameeleza kuwa Mpango Mkakati wa Wakala wa miaka mitano ijayo kuanzia mwaka huu wa 2026 ni kusimika mitambo ya aina hiyo katika Kanda zote zilizosalia nchini ambazo amezitaja kuwa ni Kanda ya Kaskazini, Kanda ya Ziwa, Kanda ya Magharibi pamoja na Kanda ya Kusini.

Hata hivyo, ameweka bayana kuwa kutokuwepo kwa mitambo ya kisasa katika Kanda tajwa haimaanishi kuwa kazi hiyo haifanyiki katika maeneo hayo, la hasha, inafanyika kwa kutumia mitambo ya ki-makenikali pamoja na ile midogo inayobebeka (Portable Test Kit) ambayo amesema Maafisa Vipimo kote nchini huibeba mikononi na kwenda nayo katika maeneo mbalimbali kuhakiki dira za maji.

Katika hatua nyingine, Biyani ametoa hamasa kwa wadau wa vipimo mkoani Dodoma na mikoa ya jirani hususani katika sekta ya maji kutumia fursa ya uwepo wa mtambo huo wa kisasa kupeleka dira za maji WMA zikahakikiwe na kuidhinishwa.

Biyani ameonya kwamba ni kosa kisheria kwa mtu yeyote kufunga na/au kutumia dira ya maji ambayo haijahakikiwa na Wakala wa Vipimo huku akibainisha kuwa adhabu yake huanzia kutozwa faini ya shilingi laki moja hadi milioni 20 kwa kosa la kwanza na shilingi milioni 20 hadi milioni 50 kwa kosa la pili kutegemea na aina ya kosa.

Ametaja gharama za kuhakiki dira za maji kwa mujibu wa sheria kuwa ni shilingi elfu kumi tu kwa kila moja na kwa uidhinishaji wa muundo ni shilingi elfu hamsini.

Sheria ya Vipimo, Sura Namba 340 kupitia kanuni zake mbalimbali inaielekeza WMA kuhakiki dira za maji walau mara moja kila mwaka lakini pia Wakala hufanya kaguzi mbalimbali za kushtukiza ili kubaini endapo kuna udanganyifu na kuchukua hatua.

Wakala imeendelea kutoa elimu kwa wadau wa vipimo na umma kwa ujumla katika maeneo mbalimbali ikiwemo namna ya kutambua kipimo ambacho kimehakikiwa ambapo kwa upande wa dira za maji, utambuzi kuwa dira husika imehakikiwa ni kwa kuona lakiri iliyofungwa pamoja na muhuri wa WMA ukionesha tarehe, mwezi na muda ambao kifaa hicho kimehakikiwa. Dira yoyote ambayo haina lakiri na muhuri wa WMA inamaanisha kuwa haijahakikiwa.

Mtambo wa kisasa unaotumika kuhakiki dira za maji. Mtambo huu wa kidijitali umefungwa katika Jengo la Makao Makuu ya Wakala wa Vipimo (WMA), Dodoma.
Sehemu ya Mtambo wa kisasa unaotumika kuhakiki dira za maji. Mtambo huu wa kidijitali umefungwa katika Jengo la Makao Makuu ya Wakala wa Vipimo (WMA), Dodoma.
Jengo lenye mitambo ya kuhakiki dira za maji, lililopo katika Kituo cha Uhakiki Vipimo Misugusugu, Mkoa wa Pwani.

Afisa Vipimo kutoka Wakala wa Vipimo (WMA), akihakiki dira za maji.


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amefanya mazungumzo na Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), Bi. Beth Bechdol jijini Dar es salaam leo tarehe 3 Februari, 2026.

Pamoja na mambo mengine, Viongozi hao wameahidi kuendeleza ushirikiano uliopo baina ya Tanzania na FAO ili kukuza na kuimarisha sekta ya Kilimo nchini.


 

Leo Jumanne, Februari 3, 2026, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ameanza ziara ya kikazi hapa Dubai, UAE kwa kufanya mazungumzo na viongozi na wadau wa kimataifa.

Katika ratiba ya leo, Rais Samia anakutana na Mhe. Gaston Browne, Waziri Mkuu wa Antigua and Barbuda, pamoja na kufanya mazungumzo ya pande mbili na Bi. Shaikha Al Nuwais, Katibu Mkuu wa Shirika la Utalii la Umoja wa Mataifa (UN Tourism), ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuimarisha ushirikiano, diplomasia ya kiuchumi na kuvutia uwekezaji wa moja kwa moja nchini.

Jioni ya leo, Rais Samia atashiriki uzinduzi wa Global Africa Investment Summit (GAIS)— jukwaa la uwekezaji linalolenga kuoanisha miradi iliyo tayari kuwekezeka barani Afrika na wawekezaji wa kimataifa.

GAIS ni mpango wa kimkakati unaoendeshwa sambamba na majadiliano ya sera ya World Governments Summit (WGS), kwa lengo la kubadili majadiliano ya sera kuwa uwekezaji halisi wenye matokeo.

Tufuatilie kupitia akaunti rasmi za Ikulu Mawasiliano kwa taarifa zaidi.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Rais wa Jamhuri ya Kossovo, Mhe. Vjosa Osmani-Sadriu, kabla ya kufanya vikao na Viongozi mbalimbali pembezoni mwa mkutano wa Jukwaa la Serikali za Dunia (WGS2026), tarehe 3 Februari, 2026 Madinat Jumeirah, Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE).
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Rais wa Jamhuri ya Angola, Mhe. João Lourenço, kabla ya kufanya vikao na Viongozi mbalimbali pembezoni mwa mkutano wa Jukwaa la Serikali za Dunia (WGS2026), tarehe 3 Februari, 2026, Madinat Jumeirah, Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE).
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiteta jambo na Rais wa Ethiopia, Mhe. Aye Atske-Selassie, kabla ya kufanya vikao na Viongozi mbalimbali pembezoni mwa mkutano wa Jukwaa la Serikali za Dunia (WGS2026), tarehe 3 Februari, 2026, Madinat Jumeirah, Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE).
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Waziri wa Nchi Umoja wa Falme za Kiarabu, Mhe. Dkt. Maitha Salem Al Shamsi muda mfupi kabla ya kufanya vikao na Viongozi mbalimbali pembezoni mwa mkutano wa Jukwaa la Serikali za Dunia (WGS2026), tarehe 3 Februari, 2026, Madinat Jumeirah, Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE).
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiondoka eneo la mkutano wa Jukwaa la Serikali za Dunia (WGS2026), tarehe 3 Februari, 2026, Madinat Jumeirah, Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE).

Na. Jacob Kasiri - Dodoma.

Timu ya wataalamu wabobezi kutoka katika Idara na Vitengo mbalimbali vya Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) wapo jijini Dodoma kuanzia Februari 02, 2026 kwa ajili ya kufanya marejeo na hatimaye kuandaa Mpango Mkakati Mpya (Strategic Plan) wa Miaka Mitano ijayo 2026/2027 - 2030/2031 baada ya Mpango Mkakati wa awali 2020/2021 - 2025/2026 kuelekea ukingoni ifikapo June 31, 2026.

Lengo la Mpango Mkakati huo ni kubainisha mwelekeo wa kimkakati na vipaumbele vya taasisi hiyo inayosimamia Hifadhi za Taifa 21, vituo vitano vya Malikale pamoja na Ofisi Viunganishi tatu za Dodoma, Dar es Salaam na Zanzibar ili kutekeleza majukumu yake kwa uwazi, uwajibikaji na kwa kuzingatia misingi ya utawala bora.

Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi - Sekela Mwangota Mkuu wa Kitengo cha Mipango, Ufuatiliaji na Tathmini - (TANAPA) ambaye ni Msimamizi Mkuu wa maandalizi ya (SP) hiyo mpya alisema,

“Mpango Mkakati huo unalenga kuongeza mazao mapya ya utalii, uimarishwaji wa ikolojia ikihusisha tiba za wanyamapori, upatikanaji wa maji ya kutosha katika Hifadhi za Taifa zinazokabiliwa kwa kiasi kikubwa na mabadiliko ya Tabianchi kama vile Mikumi, Mkomazi, Katavi na Saadani sanjari na kubuni vyanzo vipya vya mapato ili shirika liendee na shughuli zake za uhifadhi hata kama nchi itakabiliwa na majanga yatakayosababisha watalii kutokuja nchini kama ilivyotokea wakati wa Uviko 2019.”

Aidha, Kamishna Sekela aliongeza kuwa Rasimu ya Mkakati huo imejikita kuweka mifumo ya ufuatiliaji na tathmini ikianza na hali ya awali kabla ya mpango (baseline) pamoja na malengo ya kufikiwa na Idara au Kitengo kwa kila mwaka (targets). Tathmini hizo zitafanyika kwa kuangalia (ripoti ya utendaji kazi wa kila dawati, tafiti, kiwango cha kuridhika kwa wateja wetu na takwimu) lengo likiwa ni kupima kama taasisi inasonga mbele kuelekea kufikia malengo yake au la!.

Dkt. Wilhelm Kiwango Mhadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma ambaye ni mwezeshaji katika zoezi la uandaaji wa Mpango Mkakati Mpya (SP) alitanabaisha kuwa ili kupata Mpango Mkakati suluhishi utakaokidhi na kufikia malengo tarajiwa ya TANAPA, mambo muhimu yaliyoangaziwa ni pamoja na uainisha wa takwimu na uzoefu wa kitaaluma, kubaini maeneo ya kimkakati yatakayopewa kipaumbele katika miaka mitano ijayo, pamoja na matumizi bora ya rasilimali vifaa na watu ambayo itaenda sambamba na kasi ya utoaji huduma kwa wateja.

Upatikanaji wa Mpango Mkakati (SP) huo utakuwa ni mwelekeo thabiti wa TANAPA kufikia Malengo yake kuendana na mazingira ya sasa, Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, miongozo mbalimbali ya serikali inayochagizwa na sera, kanuni, mwelekeo mpya na kasi ya Wizara ya Maliasili na Utalii.




Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Fedha Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar, mazungumzo yaliyofanyika Ofisini kwa Makamu wa Rais, mkoani Dodoma leo tarehe 03 Februari 2025.


 



Stakeholders Laud Transparent Indicative Pricing System as Small Scale Output Soars


Singida

Mineral sector stakeholders in Singida Region have hailed the Singida Mineral Market as a game changer, citing significant improvements in transparency, fairness and efficiency driven by the adoption of a digital indicative pricing system.

Artisanal miners, mineral processors and traders operating in the region say the market has revolutionized mineral trade by safeguarding miners against price exploitation and quality manipulation, while strengthening trust among sector players.

Speaking at the market, a geologist from the Singida Resident Mines Office,  Mbeleye David, said the establishment of the mineral market has yielded substantial benefits for small-scale miners and traders by introducing systems that protect them from fraud related to gold quality and unfair pricing.

 David noted that before the establishment of mineral markets, Singida Region was recording very low volumes of officially traded mineral production between 100 and 200 grammes. However, through the operational mineral markets, the region is now coordinating between 50 and 60 kilogrammes of mineral output from small-scale miners, reflecting increased efficiency and stakeholder confidence in the system.

He explained that the government has put in place a robust indicative pricing mechanism aimed at protecting artisanal miners from selling minerals at undervalued prices.

“The market is equipped with a modern X-Ray Fluorescence (XRF) machine for testing gold purity, ensuring that minerals are traded based on accurate quality standards and their true market value,” said David.

He added that unlike in the past, when indicative prices were provided only for raw gold, the current system uses a digital display board showing indicative prices for various minerals, including gold, copper and silver an innovation that has enhanced transparency and eliminated loopholes for malpractice in mineral trade.

“This technology has streamlined market operations, including mineral valuation and the issuance of mineral transportation permits for both domestic and international markets, which are now processed faster and more efficiently,” he said.

Meanwhile, mineral trader   Abubakari Omary said that despite the notable progress, continuous education on the use of indicative prices is essential for miners and traders to avoid misunderstandings and disputes during transactions.

“Education remains critical to ensure every stakeholder understands their rights and obligations and conducts business based on actual market prices,” said Omary.

Stakeholders also commended the new mineral market framework for allowing unlicensed artisanal miners to register and sell their minerals directly at the markets without being required to use a trader’s licence a move that has removed a major barrier that previously limited participation in the formal mineral trade.

Overall, the Singida Mineral Market has been described as a key driver of growth in the region’s mineral sector by enhancing transparency, improving trade security and increasing government revenue through the control and prevention of mineral smuggling.

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali imepanga kununua matrekta 10,000 na kuanzisha vituo jumuishi 1,000 vya huduma za zana za kilimo katika ngazi ya Kata, hatua itakayoongeza tija, kupunguza gharama na kuwapa wakulima muda zaidi wa kushiriki shughuli nyingine za kiuchumi.

Ametoa kauli hiyo leo Jumanne, Februari 3, wakati akifungua Mkutano wa Kwanza wa Kikanda wa Afrika wa Matumizi Endelevu ya Zana za Kilimo unaofanyika katika Hotel ya Johari Rotana, Dar es Salaam ambao unalenga kuweka msingi wa ushirikiano wa kikanda katika kuendeleza Ajenda ya Mfumo wa Zana Endelevu za Kilimo Barani Afrika (F-SAMA).

Dkt. Mwigulu amesema ni muhimu kuimarisha uwekezaji katika zana za kilimo rafiki kwa mazingira na zinazozingatia mabadiliko ya tabianchi. “Zana hizi zinapaswa kupunguza uzito wa kazi, kuongeza tija, kupunguza upotevu wa mazao, na wakati huo huo kulinda mazingira kwa kutumia teknolojia zinazohimili athari za tabianchi kama ukame na mabadiliko ya misimu.”

“Tunapaswa kuhakikisha ushiriki mkubwa na wa makusudi wa Sekta Binafsi katika uzalishaji, usambazaji na utoaji wa huduma za zana za kilimo. Serikali zetu zinapaswa kuweka mazingira wezeshi ya sera, sheria na vivutio vya uwekezaji ili Sekta Binafsi iweze kushiriki kikamilifu, kuongeza upatikanaji wa zana za kilimo, na kupunguza gharama kwa wakulima.”

Waziri mkuu amesema kuwa ni lazima kuwawezesha vijana na wanawake kushiriki kikamilifu katika biashara, ubunifu na utoaji wa huduma za zana za kilimo kwa kuwa ni kundi lenye nguvu kazi, ubunifu na uwezo wa kuleta mabadiliko ya haraka endapo litapatiwa mafunzo, mitaji, teknolojia na fursa za masoko.

Amesema uwezeshaji wa makundi hayo ni msingi wa maendeleo jumuishi na endelevu. “Uwezeshaji huu unapaswa kupimwa kwa viashiria mahsusi vya ajira, uanzishwaji wa biashara endelevu, na ushiriki wa vijana na wanawake katika minyororo ya thamani ya zana za kilimo.”

Waziri Mkuu amesema kupitia mkutano huo nchi za Afrika, kwa kushirikiana na Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), Umoja wa Afrika (AU), taasisi za fedha, sekta binafsi, watafiti na wadau wa maendeleo zinakusudia kujenga mifumo thabiti ya huduma za zana za kilimo inayokidhi mahitaji halisi ya wakulima wadogo na wa kati, kuimarisha uratibu wa taasisi, kubadilishana uzoefu.

Hivyo, inatarajiwa watunga sera, wataalamu, watafiti, sekta binafsi na washirika wa maendeleo watapata fursa ya kubadilishana uzoefu, kujifunza mbinu bora, na kujenga uelewa wa pamoja kuhusu namna bora ya kuendeleza matumizi endelevu ya zana za kilimo kama chachu ya mageuzi ya mifumo ya uzalishaji chakula.

Kwa upande wake, Waziri wa Kilimo, Godfrey Chongolo amesema kuwa Kupitia mkutano huu, Serikali imepanga kuzindua Mkakati wa Taifa wa Zana za Kilimo wa Awamu ya Pili (2026-2035). Mkakati huu umelenga kuimarisha matumizi, utengenezaji, uendelezaji, uhamasishaji,usimamizi na uratibu endelevu wa teknolojia zinazorahisisha kazi na kuokoa muda katika mnyororo wa uzalishaji na uongezaji wa thamani wa mazao ya kilimo.






Na Nasra Ismail, Geita.

Baraza la Madiwani Halmashauri ya Wilaya ya Geita leo Februari 3,2026 katika Mkutano wake wa Kawaida wa robo ya pili kwa mwaka 2025/26 limewasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za maendeleo kwa ngazi ya kata.

Awali akizungumza katika baraza Hilo katika Ukumbi wa Mikutano wa Halmashauri uliopo Nzera,  Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Wilaya ya Geita Karia Rajab Magaro amewapongeza madiwani  hao kwa kupewa ridhaa na wananchi ili kuendelea kuisimamia Serikali katika utekelezaji wa shughuli za maendeleo kwa mujibu wa  Kanuni,sheria na taratibu zilizowekwa.

"Tufanye kazi kwa kushirikiana ili kuweza kufanikisha shughuli za Halmashauri" Amesema Bw. Magaro.Vilevile Magaro ametoa wito kwa Waheshimiwa Madiwani kushirikiana na watendaji katika Kata zao kufanya vikao  na kuwa na taarifa za mapato na matumizi kwa ustawi wa Halmashauri.

"Taarifa za mapato na matumizi ni muhimu sana hivyo nitoe wito kwenu kuzisimamia kwa kushirikiana na watendaji" Amesema Bw Magaro. 

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Mkutano huo ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri na Diwani wa Kata ya Nkome Mhe Christopher Kahesi amewataka Madiwani kuwa mfano mzuri kwa kuzingatia na kuzifuata kanuni,  taratibu na miongozo iliyopo ili kuwa na viwango vizuri.

Pamoja na hayo Mhe Kahesi katika Mkutano huo amewasihi Madiwani  kuendelea kutoa  ushirikiano katika kata nyingine ambazo zina changamoto ili  kuzitatua kwa ushirikiano kwa maslahi ya Halmashauri.

Mkutano huo ni wa Kwanza kwa kipindi cha robo ya pili Oktoba hadi Desemba tangu baraza  hilo lilipoingia kazini ambapo jumla ya kata 37 za Halmashauri ya Wilaya ya Geita zimewasilisha taarifa za utekelezaji wa shughuli za maendeleo kwa ngazi ya Kata.







📌 Serikali yatenga shilingi bilioni 45.6 kwa ajili ya kusambaza umeme katika vitongoji 376

📌 Kampuni ya China Railway No. 4 Engineering Group Ltd kuanza utekelezaji wa mradi mkoani Singida

📌 Wananchi zaidi ya 13,000 kunufaika na huduma ya umeme.

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, amesema kuwa utekelezaji wa mradi wa kusambaza umeme katika vitongoji 376 vya mkoa huo utawezesha uongezaji thamani wa mazao ya kilimo kupitia uanzishwaji na uendelezaji wa viwanda vidogo vidogo katika maeneo ya wananchi.

Mhe. Dendego aliyasema hayo wakati wa hafla ya kumtambulisha rasmi mkandarasi wa mradi huo, Kampuni ya China Railway No. 4 Engineering Group Ltd kutoka Jamhuri ya Watu wa China, kampuni iliyoshinda zabuni ya kusambaza umeme katika vitongoji hivyo na kuongeza kuwa mradi huo unatarajiwa kufikia kaya 13,259 mara utakapokamilika.

Amesema kuwa upatikanaji wa umeme si anasa bali ni nyenzo muhimu ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii, na kwamba Mkoa wa Singida umeendelea kupiga hatua kubwa za maendeleo kutokana na uwepo wa viwanda vidogo hadi ngazi ya vitongoji.

“Upatikanaji wa umeme utaongeza thamani ya mazao ya kilimo kupitia viwanda vidogo vidogo. Wananchi wa Mkoa wa Singida wana mahitaji makubwa ya umeme, hivyo idadi ya awali ya wananchi 13,000 ni mwanzo tu, na tunatarajia mahitaji yataongezeka zaidi,” amesema Mheshimiwa Dendego.

Aidha, Mkuu wa Mkoa huyo amemtaka mkandarasi kuhakikisha anatoa kipaumbele cha ajira za muda mfupi kwa wananchi wanaoishi katika maeneo yatakayopitiwa na mradi huo.

Mhe. Dendego alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kutoa kipaumbele katika upatikanaji wa nishati ya umeme vijijini kwa kuidhinisha jumla ya shilingi bilioni 45.6 kwa ajili ya kusambaza umeme katika vitongoji 376 vya Mkoa wa Singida.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Umeme Vijijini (REA), Mhandisi, Thomas Mmbaga, amesema kuwa Serikali kupitia REA imemtambulisha rasmi mkandarasi ili kuanza utekelezaji wa mradi huo kwa mkataba wa miaka mitatu. Ameeleza kuwa wateja wa awali 13,259 wanatarajiwa kuunganishwa na huduma ya umeme katika wilaya za Ikungi, Mkalama, Itigi, Iramba, Singida na Manyoni.

Naye mwakilishi wa Kampuni ya China Railway No. 4 Engineering Group Ltd, Mhandisi, Baraka Mhagama, amesema kuwa kampuni hiyo imejipanga kutekeleza mradi ndani ya kipindi cha miaka miwili licha ya mkataba kuruhusu utekelezaji kwa miaka mitatu. Ameahidi kushirikiana kwa karibu na REA, TANESCO pamoja na viongozi wa Mkoa wa Singida ili kuhakikisha mradi unatekelezwa kwa ufanisi na kuleta tija iliyokusudiwa.






 

Na Belinda Joseph-Arusha.

Mwenyekiti wa Ofisi ya Rais, Tume ya Utumishi wa Umma, Jaji Mstaafu Hamisa H. Kalombola, amesema kuwa usimamizi bora na ushirikishwaji wa maoteo ya bajeti kwa Taasisi za Umma ni nguzo muhimu katika kuhakikisha utekelezaji wenye ufanisi wa bajeti na mipango ya maendeleo, sambamba na kupunguza migogoro, kudhibiti mianya ya ubadhirifu na kujenga utamaduni wa uwazi na uwajibikaji.

Akizungumza leo Februari 3, 2026, Jijini Arusha, wakati wa ufunguzi as Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Tume ya Utumishi wa Umma, Jaji Mstaafu Kalombola amesema kuwa usimamizi wa fedha unaozingatia Sheria, Kanuni na Taratibu huongeza ufanisi wa matumizi ya rasilimali za umma na kuhakikisha fedha zinatumika kwa manufaa ya Taasisi na Taifa kwa ujumla.

Amesema mkutano huo umeiwezesha Tume kupitia na kujadili Makadirio ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027, pamoja na kubainisha vipaumbele vya kimkakati, maeneo yanayohitaji maboresho ya kimfumo na kiutendaji, pamoja na mpango wa matumizi ya bajeti mpya itakayokuwa dira ya utekelezaji wa shughuli za Tume.

Ameeleza uwa bajeti ni nyenzo muhimu katika utekelezaji wa mipango ya Taasisi, kwani huwezesha kupanga, kutekeleza na kutathmini shughuli kwa ufanisi, amesisitiza kuwa mjadala wa bajeti una uzito mkubwa katika kuhakikisha rasilimali zilizopo zinatumika kwa uangalifu, weledi na tija.

Ameongeza kuwa kupitia bajeti hiyo, utekelezaji wa mipango, miradi na majukumu ya kila siku ya Tume kwa mwaka ujao wa fedha utaongozwa ipasavyo, huku Tume ikiweza kubainisha vipaumbele vyake, matumizi ya rasilimali na mikakati ya kuboresha utendaji kazi.

Kwa upande wake, Kaimu Katibu wa Ofisi ya Rais, Tume ya Utumishi wa Umma, John C. Mbisso, alisema kuwa bajeti hiyo ndiyo itakayokuwa msingi wa utekelezaji wa mipango, miradi na majukumu ya Tume kwa mwaka ujao wa fedha.

Ameongeza kuwa Tume imeendelea kukua, kuboresha utendaji na kukabiliana na changamoto mbalimbali za kiutendaji, akibainisha kuwa mafanikio yaliyofikiwa hadi sasa ni matokeo ya ushirikiano wa wafanyakazi wote kuanzia ngazi ya chini hadi ya juu.

Mbisso alisisitiza kuwa mikutano ya Baraza la Wafanyakazi ni jukwaa muhimu la kubadilishana mawazo, kufanya tathmini ya pamoja na ukuhakikisha mipango ya matumizi ya fedha za umma inazingatia maslahi mapana ya Taasisi.







 


Top News