RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, leo tarehe 13 Juni 2026, amejumuika na wanafamilia, ndugu, jamaa, wasanii, na mamia ya waombolezaji katika mazishi ya msanii mkongwe, marehemu Issa Joseph Mohamed, maarufu kwa jina la Mzee Onyango, yaliyofanyika Kawe , Wilaya ya Kinondoni, Jijini Dar es Salaam.

Mazishi hayo yamehudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, akiwemo Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma, pamoja na wasanii wa fani mbalimbali na wananchi waliofika kutoa heshima zao za mwisho kwa marehemu.

Mara baada ya kuwasili, Rais Dkt. Mwinyi alisaini kitabu cha maombolezo na kutoa mkono wa pole kwa wanafamilia.

Marehemu Issa Joseph Mohamed alizaliwa tarehe 14 Aprili 1950 na kufariki dunia tarehe 11 Juni 2026, akiwa anapatiwa matibabu katika Hospitali ya Jeshi ya Lugalo, Jijini Dar es Salaam.

Wakati wa uhai wake, marehemu alipata umaarufu mkubwa kupitia kazi zake za filamu na maigizo na kujizolea heshima kubwa miongoni mwa Watanzania kwa jina la Mzee Onyango.

Marehemu amezikwa katika Makaburi ya Kondo, Ununio, Wilaya ya Kinondoni, Jijini Dar es Salaam.
Bwana ametoa na Bwana ametwaa; jina la Bwana lihimidiwe. Amina.
























Na Mwandishi Wetu, Temeke
JAMII imetakiwa kuongeza juhudi za kulinda haki za watoto na kuhakikisha wanapata mazingira salama ya kukua bila ukatili.

Wito huo umetolewa na Mwenyekiti wa UWT Wilaya ya Temeke, Lawama Mikidadi, ambaye alikuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika yaliyofanyika wilayani humo.

Mikidadi amesema maadhimisho hayo ni nafasi ya kuikumbusha jamii wajibu wake wa kusimamia ustawi wa watoto.

“Licha ya jitihada zinazofanywa, bado kuna matukio ya ukatili dhidi ya watoto katika baadhi ya maeneo. Ni wajibu wa wazazi, walezi na jamii kwa ujumla kuhakikisha vitendo hivyo vinatokomezwa,” amesema.

Maadhimisho ya mwaka huu yamefadhiliwa na taasisi za Boys Initiative Tanzania na Miriam Odemba Foundation, ambazo zimetoa pedi na vifaa mbalimbali kwa watoto 300 walioshiriki.

Kwa upande wake, halmashauri ya Manispaa ya Temeke imadhimisha siku hiyo mapema kabla ya tarehe 16 juni mwaka huu.

Kupitia ushiriki huo, Boys Initiative Tanzania imeendelea kupaza sauti ya mtoto wa kiume, huku Miriam Odemba Foundation ikisimama kutetea na kuwezesha mtoto wa kike, taasisi zote mbili zikifanya kazi ya kuhakikisha watoto wanapata ulinzi, fursa na mazingira bora ya kufikia ndoto zao.

Akizungumza na wanafunzi, Mrakibu Msaidizi wa Polisi kutoka Dawati la Jinsia na Watoto Wilaya ya Temeke, Brandina Ndunguru, amewataka watoto kuwa makini dhidi ya watu wanaoweza kutumia zawadi au ahadi mbalimbali kuwashawishi.

“Mtoto anapaswa kulindwa, kusikilizwa na kupewa nafasi ya kueleza changamoto zake. Wazazi wajenge urafiki na watoto wao ili waweze kuwasaidia kwa karibu zaidi,” amesema.

Kwa upande wake, Mratibu wa Maendeleo ya Mtoto wa Halmashauri ya Manispaa ya Temeke, Sweetbertha Pascal, amesema halmashauri imeendelea kutoa elimu ya malezi bora na kupinga ukatili wa kijinsia katika shule na mitaa yote 42 ya manispaa hiyo.

Watoto walioshiriki maadhimisho hayo pia wamesema elimu waliyoipata imewasaidia kuelewa haki zao na namna ya kujilinda.

“Sasa tunajua umuhimu wa kutoa taarifa tunapoona au kufanyiwa vitendo visivyofaa ili tupate msaada kwa wakati,” amesema Edwin John kwa niaba ya wanafunzi.

Maadhimisho hayo yalishirikisha shule sita, walimu, viongozi wa serikali na wadau wa maendeleo ya watoto, yakibeba kaulimbiu isemayo “Mtoto ni Malezi, Msingi wa Familia Bora kwa Taifa Imara.”







Kaimu Mkurugenzi Mtendaji  Bank of Africa, Wasia Mushi ( wa pili kulia mstari wa pili, Mkuu wa Fedha Stivin Mwanjibili (wa pili kutoka kushoto mstari wa mwisho)   walijumuika na watendaji waandamizi wa taasisi nyingine kusikiliza hotuba ya Bajeti ya Kuu ya Serikali ya Mwaka 2026/2027 iliyosomwa na Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar,bungeni Dodoma mwishoni mwa wiki.


BANK Africa Tanzania imeipongeza Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2026/2027 yenye thamani ya shilingi trilioni 62.3, ikisema inalenga kuharakisha utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na Mpango wa Nne wa Maendeleo ya Taifa huku ikichochea ukuaji wa uchumi na uwekezaji nchini.

Benki hiyo pia imeeleza dhamira yake ya kuendelea kuboresha huduma kwa wateja binafsi, wafanyabiashara wadogo na wa kati (SMEs) pamoja na makampuni makubwa ili kuunga mkono ajenda ya Serikali ya kuimarisha ushirikishwaji wa kifedha.

Akizungumzia bajeti hiyo iliyowasilishwa bungeni na Waziri wa Fedha, Dk. Khamis Mussa Omar, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Bank of Africa Tanzania, Wasia Mushi, alisema bajeti ya mwaka huu imeweka mazingira mazuri kwa wawekezaji na wafanyabiashara kwa kuimarisha mageuzi ya kidijitali, kuvutia uwekezaji na kujenga uchumi himilivu na jumuishi.

“Kuongezeka kwa ushiriki wa sekta binafsi katika uwekezaji na biashara ni ishara kwamba Serikali ya Awamu ya Sita imejipanga kuleta mageuzi ya kiuchumi yanayowanufaisha Watanzania wengi zaidi,” alisema Mushi.

Alisema benki hiyo imevutiwa na hatua za Serikali za kuboresha mazingira ya biashara kupitia kupunguza urasimu, kurekebisha mfumo wa kodi na kuondoa migongano ya majukumu katika taasisi za umma.

Kwa mujibu wake, uwekezaji unaoendelea katika miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo Reli ya Kisasa (SGR), barabara na nishati utaongeza mzunguko wa fedha, kuchochea shughuli za sekta binafsi na kuunda fursa zaidi za ajira.

Mushi alisema bajeti hiyo pia itasaidia kuvutia uwekezaji wa ndani na nje, kupanua wigo wa kodi, kuongeza ajira na kuhamasisha ulipaji wa kodi kwa hiari. Aidha, alibainisha kuwa Serikali imeendelea kutambua mchango wa sekta binafsi kama nguzo muhimu ya ukuaji wa uchumi na utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Aliongeza kuwa juhudi za kurasimisha sekta isiyo rasmi zitasaidia wafanyabiashara kupata masoko, huduma za kifedha, mikopo na bima, hatua itakayochochea zaidi ukuaji wa uchumi.

Mushi alisema Serikali imeendelea kutekeleza sera za fedha na bajeti zinazowezesha sekta binafsi kwa kuboresha mazingira ya biashara, kulinda thamani ya shilingi na kuongeza ukusanyaji wa mapato.

Kwa upande wa benki hiyo, alisema Bank of Africa Tanzania inaendelea kuwa imara kimtaji na kuendesha shughuli zake kwa kuzingatia kanuni za mamlaka za usimamizi wa sekta ya fedha. Hivi karibuni benki hiyo imezindua tawi maalumu la wajasiriamali (SME Hub) pamoja na programu za huduma za kifedha na ushauri kwa wafanyabiashara wadogo na wa kati.

Alisema hatua hizo zinalenga kuboresha upatikanaji wa mikopo, kuongeza elimu ya biashara na kuimarisha ushindani wa kibiashara nchini.

 Benki ya NMB imesisitiza umuhimu wa kupeleka elimu ya fedha kwa umma sambamba na kupanua huduma rasmi za kifedha, ikisema ujumuishaji wa kifedha unahitaji vijana kuelewa kuweka akiba, kupanga matumizi, kutumia huduma za kidijitali kwa usalama na kukopa kwa uwajibikaji.

Akizungumza katika Tamasha la Twen’Zetu kwa Yesu 2026 katika Viwanja vya Tanganyika Packers, Kawe, Dar es Salaam, Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB, Filbert Mponzi, alisema vijana wanapaswa kujifunza kusimamia fedha zao mapema na kutumia teknolojia pamoja na vipaji vyao kujenga vyanzo vya kipato.

Katika tamasha hilo, NMB ilitoa elimu kuhusu akiba, mikopo, bima na huduma za kidijitali. Tawi Linalotembea la NMB—Bank on Wheels—pamoja na mawakala wa benki hiyo pia walitoa huduma za kifedha, zikiwemo kufungua akaunti na kufanya miamala.

Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Askofu Dkt. Alex Gehaz Malasusa, aliwataka vijana kuunganisha fursa za kiuchumi na maadili, huku mshiriki Jennifer Minja akisema mafunzo hayo yameongeza uelewa wake kuhusu umuhimu wa akaunti, akiba na matumizi yanayowajibika ya mikopo.

Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Askofu Dk. Alex Malasusa (kushoto), akizungumza na Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB Bank Plc, Filbert Mponzi (wa pili kulia), na Mkuu wa Mauzo na Mtandao wa Matawi wa NMB, Donatus Richard (wa pili kushoto), mara baada ya kuzindua rasmi Tamasha la Twen’Zetu kwa Yesu katika Viwanja vya Tanganyika Packers, Kawe, Dar es Salaam. Kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Upendo Media, Neng’ida Johanes. NMB ilikuwa mdhamini mkuu wa tamasha hilo.











Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kulinda uhuru wa kuabudu na kuimarisha ushirikiano na taasisi za dini kwa kutambua mchango mkubwa unaotolewa na taasisi hizo katika kujenga maadili, amani, mshikamano na maendeleo ya Taifa.

Dkt. Mwigulu amesema hayo leo, Jumapili Juni 14, 2026, aliposhiriki Ibada katika Kanisa la Tanzania Assemblies of God (TAG) Kiomboi Christian Centre, mjini Kiomboi, Wilaya ya Iramba mkoani Singida.

Ibada hiyo iliongozwa na Askofu wa Jimbo la Singida Kaskazini, Dkt. Danford Obadia pamoja na Mchungaji Kiongozi wa Kanisa hilo, Yona Suleman Essya.

Akizungumza na waumini hao, Waziri Mkuu amesema Serikali inatambua nafasi muhimu ya taasisi za dini katika malezi ya jamii na kwamba itaendelea kuweka mazingira rafiki yatakayowezesha taasisi hizo kutekeleza majukumu yake kwa uhuru na ufanisi.

“Sisi wote tutaendelea kulinda mazingira bora ya kuendesha ibada. Serikali itaendelea kutambua na kuamini kazi inayofanywa na taasisi za dini katika kujenga Taifa letu,” amesema Dkt. Mwigulu.

Amesema taasisi za dini zimekuwa mshirika muhimu wa Serikali katika kujenga maadili mema, kuhimiza uwajibikaji, kuimarisha mshikamano wa kijamii na kupambana na vitendo vinavyokinzana na utu na maendeleo ya wananchi.

Waziri Mkuu amesema Kanisa la TAG limekuwa na mchango mkubwa katika kuelimisha jamii, kuondoa imani potofu na kuhamasisha wananchi kuzingatia maadili na misingi sahihi ya maisha.

“TAG haikusimama kwenye ibada pekee, bali imebadilisha hata maisha ya kila siku ya wananchi. Imechangia kuondoa baadhi ya mila na imani zilizokuwa zinarudisha nyuma maendeleo ya watu wetu,” amesema.

Wakati huo huo, Dkt. Mwigulu ametoa rai kwa wananchi kuendelea kuheshimu nyumba za ibada na kuepuka kuziingiza katika shughuli zinazoweza kuvuruga dhamira na malengo yake ya msingi.

“Ukitaka siasa anzisha chama cha siasa. Usipeleke fujo kwenye nyumba ya ibada. Lazima tuendelee kuheshimu utakatifu wa nyumba zetu za ibada,” amesema.

Aidha, Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kupokea ushauri na maoni kutoka kwa viongozi wa dini ili kuboresha zaidi mazingira ya utoaji huduma kwa wananchi na kuimarisha maendeleo ya Taifa.

Awali akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na waumini, Askofu wa Jimbo la Singida Kaskazini, Dkt. Danford Obadia amesema kanisa linaendelea kumuombea Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na viongozi wa Serikali ili waendelee kutekeleza majukumu yao kwa hekima, uadilifu na mafanikio kwa manufaa ya Taifa.

Askofu Obadia amesema Watanzania wana wajibu wa kuliombea Taifa na viongozi wake kwa mujibu wa mafundisho ya Biblia ili nchi iendelee kudumisha amani, utulivu na maendeleo.

“Kabla ya mambo yote, nataka dua na sala na maombezi yafanyike kwa ajili ya wafalme na wenye mamlaka, ili tuweze kuishi kwa amani na utulivu. Hii nchi ni ya kwetu; tukiipenda nchi yetu na kuwaombea viongozi wetu, tutakaa nchi hii salama na tutaondoka duniani salama,” amesema Askofu Obadia.







Top News