Na Mwandishi Wetu, Arusha

Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi, leo Aprili 30, 2026, “amewapiga msasa” waongoza watalii zaidi ya 230 wa kozi ya sita katika mfululizo wa mafunzo kwa wataalamu hao kuwaongezea uwezo zaidi wa kuhudumia wageni katika semina inayoendelea jijini Arusha katika Ukumbi wa AIM Mall.

Dkt. Abbasi ametoa mada kuhusiana na Majukumu ya Waongoza Watalii katika Kulinda Chapa (Branding) ya Nchi iliyobeba anuani ya: “ National/ Destination Branding and the Role of Tour Guides.” 

Katibu Mkuu huyo ambaye pia ni mtaalam wa masuala ya mawasiliano kwa umma, ametoa mfano wa mafanikio ya filamu ya “Tanzania: The Royal Tour” kuwa moja ya ushuhuda wa umuhimu wa nchi kuwekeza katika mikakati mikubwa ya kuiweka chapa yake katika ramani ya dunia.

“Sote hapa tutakiri kuwa Royal Tour ilifanikiwa sana na inabaki kuwa moja ya miradi yetu mikubwa kama Taifa ya kuitangaza Tanzania uliolipa sana. Nawahakikishieni tunakuja na mipango zaidi ya kuipeleka chapa ya Tanzania kimataifa zaidi,” alisema.

Amewapa mifano mbalimbali waongoza watalii hao jinsi nchi nyingi duniani zinavyowekeza katika kusambaza  habari nzuri na vivutio vyao vya utalii zaidi badala ya kulalamika au kuainisha changamoto zaidi.

“Kuna nadharia (theory) katika mawasiliano kwa umma inasema mtu akilitangaza jambo sana na kulirudiarudia (agenda setting) hata kama ni la uongo litaanza kuaminika. 

Sisi ni mabalozi wa utalii basi tukayaoneshe na kuyasema mazuri ya vivutio vyetu badala ya kuposti vitu vidogo vidogo vyenye changamoto,” alisema akionesha mifano ya baadhi ya nchi zinavyotumia nguvu kubwa kutangaza vivutio vyao japo ni vichache na haviizidi Tanzania. 

Mafunzo hayo yameandaliwa na Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kushirikiana na Chama cha Wamiliki wa Kampuni za  Utalii Tanzania(TATO) na yanafanyika kwa awamu (batches) kadhaa zenye washiriki zaidi ya 250 kila moja na lengo ni kuwafikia waongoza watalii zaidi ya 2,500 ikiwa ni maandalizi ya msimu mpya wa utalii lakini na matukio makubwa kama Afcon 2027.

Kwa mujibu wa takwimu za Benki Kuu ya Tanzania, watalii wa kimataifa nchini wameongezeka kutoka 922,000 mwaka 2021 kabla ya Royal Tour na kufikia 2,294,000 mwaka jana huku mapato ya jumla ya sekta ya utalii yakifikia Dola Bilioni 4.4 kutoka Bilioni 1.3 mwaka 2021 kabla ya Royal Tour.








Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2026, Ndugu Wazo Mwang’onda, ameipongeza TARURA wilaya ya Ruangwa kwa usimamizi mzuri wa mradi wa barabara ya Mwilala yenye urefu wa kilomita 0.59 kwa kiwango cha lami.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa barabara hiyo, Mwang’onda alisema ameridhishwa na ubora wa ujenzi huo ambao umejumuisha mitaro na kusimamiwa kwa viwango bora. 

Meneja wa TARURA wilaya ya Ruangwa, Mhandisi Mashaka Nalupi alisema mradi huo uliojengwa na M/S JATL TECH & CONSTRUCTION COMPANY LIMITED umegharimu shilingi 513,320,500.00.

Lengo la mradi ni kuboresha usafirishaji kwa wakazi wa vijiji vya Likangara, Dodoma, Nachingwea na Mchanganindani. Mhandisi Nalupi aliongeza kuwa barabara ya lami imepunguza kwa kiasi kikubwa gharama za ukarabati wa mara kwa mara.

Wananchi wa Ruangwa wamesema barabara hiyo imeleta faraja, kwani sasa wanaweza kufanya biashara hata nyakati za usiku kutokana na kuwepo kwa taa za barabarani. 








WWakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA) umechukua hatua madhubuti ya kuhamasisha matumizi ya nishati safi kwa kuwagawia watumishi wake majiko ya umeme, ikiwa ni sehemu ya juhudi za makusudi za kuhamasisha mabadiliko ya matumizi ya nishati nchini.

Akizungumza katika tukio hilo, Mkurugenzi wa Uendeshaji wa PBPA, Mhandisi Bruno Tarimo, amesema hatua hiyo inalenga kuimarisha juhudi za taasisi katika kuelimisha jamii kuhusu matumizi ya nishati safi na salama kwa matumizi ya kila siku.

Ameeleza kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia sera mbalimbali za kitaifa na kimataifa, imeendelea kutambua umuhimu wa nishati safi ya kupikia kama nyenzo muhimu ya kukabiliana na changamoto za kimazingira, kiafya, kijamii na kiuchumi.

“PBPA inatekeleza jukumu muhimu katika kusaidia juhudi za Serikali za kuhakikisha asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034. Ugawaji wa majiko janja aina ya pressure cooker kwa watumishi ni sehemu ya mkakati huo,” amesema Tarimo.

Aidha, amewataka wanufaika wa majiko hayo kuyatumia ipasavyo na kuwa mabalozi wa kuhamasisha matumizi ya nishati safi katika jamii zao ili kuongeza uelewa na kuharakisha mabadiliko ya matumizi ya nishati nchini.

Kwa upande wake, Afisa Dawati wa Nishati Safi ya Kupikia kutoka PBPA, Bi. Hilda Kowero, amesema kuwa Serikali imeweka mkakati maalum wa nishati safi ya kupikia unaolenga kuboresha maisha ya wananchi kupitia matumizi ya teknolojia rafiki kwa mazingira.

Amefafanua kuwa matumizi ya majiko ya umeme husaidia kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa, hivyo kulinda misitu, kupunguza ukataji wa miti na kuboresha afya kwa kupunguza madhara ya moshi yanayosababisha magonjwa ya njia ya hewa.

Katika kuhakikisha matumizi sahihi na salama ya majiko hayo, watumishi walipatiwa mafunzo maalum kuhusu namna bora ya kuyatumia, kutunza na kuzingatia tahadhari za usalama. Mafunzo hayo yalijumuisha matumizi sahihi ya umeme, njia za kupunguza matumizi ya nishati, pamoja na mbinu za kupika kwa ufanisi kwa kutumia majiko ya shinikizo (pressure cooker). Hatua hiyo inalenga kuwajengea watumishi uelewa wa kina ili waweze kunufaika kikamilifu na teknolojia hiyo na kueneza maarifa hayo kwa jamii inayowazunguka.

Bi. Kowero ameongeza kuwa PBPA itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhamasisha mabadiliko ya tabia kwa wananchi ili kuongeza matumizi ya nishati safi na kuchangia katika ujenzi wa jamii yenye afya bora na mazingira endelevu. 






Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.), ameagana na Balozi mteule wa Tanzania katika Jamhuri ya Korea Mhe. Balozi Noel E. Kaganda. 

Akizungumza katika kikao hicho kilichofanyika tarehe 30 Aprili, 2026 katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam, Waziri Kombo amemsii Balozi Kaganda kuendeleza ushirikiano wa kimkakati uliopo baina ya Tanzania na Jamhuri ya Korea, hususan katika sekta za uchumi wa buluu, elimu, miundombinu, teknolojia, viwanda, biashara, uwekezaji, afya na utalii. 

Aidha, amemsisitiza kufuatilia utekelezaji wa makubaliano yote yaliyofikiwa baina ya nchi hizi mbili, ikiwemo utekelezaji wa miradi iliyosainiwa wakati wa ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, mwezi Juni 2024.

Kwa upande wake, Balozi Kaganda amemshukuru Waziri Kombo kwa nasaha na miongozo yake na kuahidi kutekeleza diplomasia ya uchumi kwa vitendo kwa maslahi ya taifa. 

Kikao hicho pia kilihudhuriwa na Katibu Mkuu wa Wizara, Balozi Dkt. Samwel W. Shelukindo, ambaye aliungana na Waziri Kombo kumtakia Balozi Kaganda uwakilishi mwema huko Seoul, Jamhuri ya Korea.





Mkuu wa Maliasili kupitia Ujumbe wa Umoja wa Ulaya Bw. Lamine Diallo (katikati) akizindua rasmi Wito wa Tano wa Ufadhili wa Kichocheo wa Programu ya FUNGUO Jijini Dar es Salaam.Wengine kutoka kushoto ni Meneja wa Programu ya FUNGUO Bw. Joseph Manirakiza, mwakilishi wa UK FCDO, Bw. Euan Davidson, Mkuu wa Ushirikiano katika Ubalozi wa Finland, Bi. Sana-Liis Taivalmaa na Naibu Mwakilishi Mkazi wa UNDP Bw. John Rutere.


· Yazindua Wito wa 5 wa Ufadhili wa Kichocheo

SHIRIKA la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Maendeleo (UNDP), kupitia Mpango wa Ubunifu wa FUNGUO, imehitimisha kwa mafanikio Hafla ya Tuzo za #YouthIgnite Awamu ya Tatu na Uzinduzi wa Wito wa 5 wa Ufadhili wa Kichocheo wa FUNGUO, ikiashiria hatua muhimu katika kuimarisha ujasiriamali unaoongozwa na vijana na mifumoya ubunifu katika vyuo vikuu vya Tanzania.

Katika hafla hiyo, FUNGUO ilitunuku biashara 20 zilizoanzishwa na wanafunzi chini ya mpango wa #YouthIgnite Student Founders Fellowship wa awamu ya tatu. Hatua hii inaleta jumla ya biashara zilizoungwa mkono kufikia 60 kupitia awamu tatu, na kuonyesha ukuaji wa mchango wa vyuo vikuu katika uundaji wa ajira na maendeleo ya uchumi.

Meneja wa Mradi wa FUNGUO, Bw Joseph Manirakiza, alitangaza kuongezeka kwa msaada kwa vituo saba vipya vya ubunifu vinavyotegemea vyuo vikuu, na hivyo kufikisha jumla ya vituo vinavyoungwa mkono kote nchini kufikia 17.

“Vituo hivi vina mchango muhimu katika kulea wajasiriamali wachanga kupitia mafunzo, ushauri elekezi, ujasiriamali shirikishi, na upatikanaji wa rasilimali za awali,” alisema.

Hafla hiyo pia ilishuhudia uzinduzi rasmi wa Wito wa 5 wa Ufadhili wa Kichocheo wa FUNGUO, unaolenga biashara bunifu na changa zinazofanya kazi kwenye mnyororo wa thamani wa kilimo, ubunifu wa kidijitali, na madini muhimu—sekta zilizopewa kipaumbele katika maendeleo ya taifa.

Bw. Manirakiza aliendelea kusema kuwa tangu kuanzishwa kwake, FUNGUO imewekeza zaidi ya shilingi bilioni 7.5 katika biashara changa bunifu (startups) 88 na kusaidia zaidi ya nusu ya biashara hizo kuvutia zaidi ya shilingi bilioni 18 za mitaji ya ziada. Kwa pamoja, biashara hizi zimechangia kuzalisha na kudumisha zaidi ya ajira 10,000 nchini Tanzania.

Mpango wa FUNGUO unatekelezwa na UNDP Tanzania kwa ushirikiano na ANZA Entrepreneurs, kwa msaada wa Umoja wa Ulaya, Serikali ya Finland, na UK FCDO.

Akizungumza katika hafla hiyo, Naibu Mwakilishi Mkazi wa UNDP Tanzania Bw. Jouhn Rutere alisema, “ Kwa kuwekeza katika wanafunzi wa vyuo vikuu nchini, FUNGUO inasaidia kufanya vyuo vicochee ujasiriamali na kuongeza ajira. Hii inadhihirisha kinachowezekana pale ambapo kuna uwezeshaji kifedha, ushirikiano na ubunifu vinaunganishwa pamoja.”

Naye Mwakilishi wa Umoja wa Ulaya, Bw Lamine Diallo alisema EU inajivunia kuiwezesha program ya FUNGUO ambayo inawezesha vijana kubadili mawazo yao ya kibunifu kuwa biashara. “Kufadhili ubunifu unaoongozwa na wanafunzi na sekta nyeti kama kilimo, ubunifu wa kidijitali na madini muhimu kunahitajika ili ukuaji wa uchumi uwe endelevu.

Kwa upande wake, mwakilishi wa UK FCDO, Bw. Euan Davidson naye alisema, kupitia program hii ya FUNGUO, tunashuhudia ni namna gani uwezeshaji wa kifedha unaweza kuchochea uwekezaji binafsi, kukuza ajira na kusaidia biashara ambao zinaashiria dalili njema. Uzinduzi wa Wito wa 5 wa Ufadhili ni hatua muhimu katika kuwezesha ukuaji wa ubunifu Tanzania.”

JESHI la Polisi Mkoa wa Rukwa limewakamata watu wawili kwa tuhuma za kuwafanyia vitendo vya ukatili watoto, ikiwemo kuwachoma moto na kuwasababishia majeraha makubwa, katika matukio tofauti yaliyotokea wilayani Kalambo na Sumbawanga.

Watuhumiwa hao ni Fortunatus Benezet Mawela (60), mkazi wa kijiji cha Singiwe, Wilaya ya Kalambo, pamoja na Aisha Credo Mpepo (25), mkazi wa kitongoji cha Kasanzama, mji mdogo wa Laela, Wilaya ya Sumbawanga. Inadaiwa kuwa Aprili 19, 2026, Mawela alimchoma moto mjukuu wake wa kiume mwenye umri wa miaka 16 katika maeneo ya tumbo na mapaja, huku akiwa amemfunga mikono na miguu, akimtuhumu kumuibia ndizi.

Katika tukio jingine lililotokea Aprili 27, 2026, Aisha Credo Mpepo anadaiwa kumuunguza mgongoni mtoto wake wa kiume mwenye umri wa miaka 8 kwa kutumia pasi ya umeme, akimtuhumu kumuibia shilingi 2,000 zilizokuwa zimepangwa kwa ajili ya kununulia mkaa.

Jeshi la Polisi limeeleza kuwa taratibu zinaendelea kukamilishwa ili watuhumiwa hao wafikishwe mahakamani kujibu tuhuma zinazowakabili.

Wakati huo huo, Mahakama ya Wilaya ya Kalambo imemhukumu Bosco John Fatachi (38), mkazi wa kijiji cha Kambo, kulipa faini ya shilingi 300,000 au kutumikia kifungo cha miaka mitatu jela baada ya kupatikana na hatia ya kumfanyia ukatili mtoto wa miaka 8. Mshtakiwa huyo alithibitika kumpiga mtoto huyo kwa waya wa umeme huku akiwa amemfunga mikono na miguu kwa kamba, akimtuhumu kumuibia pipi zenye thamani ya shilingi 200.

Aidha, Mahakama iliyoongozwa na Hakimu Nickson Temu iliamuru mshtakiwa kulipa fidia ya shilingi 500,000 kwa mtoto huyo, ikisisitiza kuwa adhabu hiyo iwe fundisho kwa jamii dhidi ya vitendo vya ukatili kwa watoto.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Rukwa limelaani vikali vitendo hivyo na kutoa wito kwa wazazi na walezi kuacha kutoa adhabu za kikatili, badala yake kuzingatia malezi bora na yenye kuzingatia haki za mtoto. Pia limewapongeza wananchi wanaoendelea kutoa taarifa zinazosaidia kufichua vitendo vya ukatili majumbani.


Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam Rais Mstaafu Dkt Jakaya Mrisho Kikwete akiwa na Mkuu wa Harvard Kennedy School, Prof. Jeremy M. Weinstein baada ya mazungumzo yao huko Marekani)

CHUO Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kimeingia katika mazungumzo ya ushirikiano wa kimkakati na Chuo Kikuu cha Harvard, Marekani, yakilenga kuimarisha matumizi ya Akili Mnemba (AI) katika elimu, utafiti na uchambuzi wa taarifa.

Mazungumzo hayo yalianzishwa na Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, alipokuwa katika ziara ya kikazi nchini Marekani.

Ushirikiano huo unalenga kujenga uwezo wa kutumia AI kwa ufanisi katika kufundishia, kuongeza kasi ya tafiti, na kurahisisha uchakataji wa taarifa nyingi kwa wakati mfupi, eneo ambalo linazidi kuwa muhimu katika vyuo vikuu duniani.

Katika kipindi ambacho taasisi za elimu ya juu zinakabiliana na changamoto na fursa zinazotokana na AI, hatua ya UDSM kuingia katika mazungumzo na Harvard inaonekana kama mkakati wa mapema wa kuhakikisha Tanzania haiwi nyuma katika mapinduzi ya teknolojia.

Akizungumza katika kikao hicho, Dkt. Kikwete alisisitiza umuhimu wa matumizi sahihi na yenye uwajibikaji ya AI, akibainisha kuwa teknolojia hiyo inaweza kuwa nyenzo muhimu ya kuboresha ubora wa elimu na utafiti iwapo itasimamiwa vyema.

Kwa upande wa Harvard, majadiliano yalihusisha viongozi na wataalamu waandamizi, akiwemo Mkuu wa Harvard Kennedy School, Prof. Jeremy M. Weinstein, pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Maendeleo ya Kimataifa (CID), Dkt. Fatema Sumar.

Aidha, timu ya wataalamu wa AI kutoka Harvard ilishiriki majadiliano hayo, wakiongozwa na Prof. Sharad Goel, akishirikiana na Dkt. Dan Levy na Dkt. Teddy Svoronos—wote wakiwa na uzoefu mkubwa katika matumizi ya AI katika sera za umma na uchambuzi wa data.

Ushirikiano huu unatarajiwa kufungua ukurasa mpya katika sekta ya elimu ya juu nchini, kwa kuunganisha utaalamu wa ndani na uzoefu wa kimataifa katika matumizi ya teknolojia ya kisasa.

-Bilioni 3.2 kutumika kukamilisha miradi Ludewa, Njombe

-Wananchi, taasisi za kijamii kuanza kunufaika na nishati ya REA

-Sekta za uvuvi, afya na elimu kupata mapinduzi makubwa


Ludewa, Njombe📍

Matumaini ya ukuaji wa uchumi na uboreshaji wa huduma za kijamii yameongezeka kwa wakazi wa mwambao wa Ziwa Nyasa, wilayani Ludewa, kufuatia hatua ya Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kufikisha miradi ya umeme kwenye vitongoji vya eneo hilo.

Katika ziara ya Bodi ya Nishati Vijijini (REB) iliyolenga kukagua maendeleo ya miradi hiyo mkoani Njombe, imebainika kuwa kiasi cha Shilingi Bilioni 3.2 kimetengwa kwa ajili ya kukamilisha miradi ya kusambaza nishati hiyo katika wilaya ya Ludewa.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo katika Shule ya Msingi Lumbila, Mwalimu Mkuu Msaidizi, John Mwasoso, amesema ujio wa umeme ni ukombozi katika mazingira ya kufundishia na kujifunzia. Alibainisha kuwa tayari wameanza maandalizi ya awali kwa kufanya mifumo ya nyaya (wiring) kwenye baadhi ya vyumba vya madarasa na nyumba za walimu.

Kwa upande wao, wananchi wa kitongoji cha mabatini wameonyesha shauku ya kutumia nishati hiyo kuchochea uchumi wao, hususan katika sekta ya uvuvi. Bwana Augustino Madesu, mkazi wa eneo hilo, alisema umeme utawasaidia kuhifadhi samaki kwa kutumia majokofu (friza), jambo litakalowaepushia hasara ya kuuza samaki kwa bei ya kutupa pindi wanapovua kwa wingi.

Naye Mganga Mfawidhi wa zahanati ya Nkanda, Timotheo Nkwabi, alieleza kuwa umeme utamaliza changamoto ya kutoa huduma za afya gizani wakati wa usiku na kuimarisha mifumo ya kidigitali ya utunzaji wa kumbukumbu za wagonjwa na dawa.

Mkurugenzi wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Mhandisi, Ahmed Chinemba, amewahakikishia wananchi kuwa serikali imeweka kipaumbele kwenye taasisi za umma kama shule, zahanati na miradi ya maji ili kuhakikisha wananchi wananufaika kwa haraka.

“Tunawahamasisha wananchi kujiandaa kwa kufanya ‘wiring’ kwenye majengo yao ili waweze kuupokea umeme mara tu unapofika. Lengo ni kuona nishati hii inabadilisha maisha ya mtanzania wa vijijini,” alisema Mhandisi, Chinemba.

Naye Kaimu Meneja Msimamizi wa Miradi REA, Mhandisi Deogratius Nagu, aliongeza kuwa kutokana na ongezeko la mahitaji, Bodi ya Nishati Vijijini (REB) imeelekeza kuongezwa kwa idadi ya wanufaika ili kuhakikisha kaya nyingi zaidi zinapata nishati hiyo kabla ya mradi kukamilika rasmi.

Kukamilika kwa mradi huu kunatarajiwa kufungua fursa mpya za ajira kwa vijana kupitia vijiwanda vidogo, saluni, na biashara nyinginezo zinazotegemea nishati ya umeme, huku kukiimarisha usalama na ustawi wa jamii katika mwambao wa Ziwa Nyasa.





Na Mwandishi Wetu

KAMPUNI ya Oryx Gas Tanzania imesema mkakati wake ni kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia huku pia ikisisitiza umuhimu wa elimu ya mara kwa mara kwa watumiaji ili wawe na uelewa namna bora ya kutumia nishati safi ya kupikia

Hivyo katika kufanikisha mkakati huo Oryx Gas imesema imeamua kuanzisha maduka maalum yatakayotumika kuhamasisha wananchi kutumia nishati safi kwa kusogeza huduma hiyo karibu lakini wakati huo huo maduka hayo yatatumika kutoa elimu ya matumizi bora na salama ya nishati safi.

Akizungumza leo Aprili 30,2026 wakati wa ufunguzi wa duka maalum la kuuza mitungi ya Gesi ya Oryx lililopo eneo la Banana jijini Dar es Salaam Menaja Masoko na Mauzo Shaban Fundi amesema wanatambua juhudi za serikali katika kuhimiza nishati safi.

“Sisi Oryx Gas ni vinara wa nishati safi ya kupikia hivyo tumeunganisha nguvu zetu kwa kuunga mkono jitihada za Serikali kuhakikisha matumizi ya nishati safi ya kupikia yanafika kwa wananchi wote.Tunatambua namna gani Serikali inatamani ifikapo mwaka 2030 basi asilimia 80 ya Watanzania iwe inatumia nishati safi ya kupikia 

“Kwahiyo ufunguzi wa maduka haya maalum ni muendelezo wa muunganiko wetu kuunga mkono juhudi za Serikali na wananchi kwa ujumla kwamba nishati safi sio anasa bali ni lazıma kwamba watu wapate nishati safi ya kupikia na sisi kama Oryx tumeendelea kuboresha miundombinu ya kuhifadhi ,kupokea pamoja na usambazaji lengo ni kuona huduma inafika kwa jamii.”

Kuhusu elimu ya namna bora ya kutumia nishati safi ya kupikia amesema ni jambo la msingi wananchi kujengewa uelewa kuhusu matumizi ya nishati hiyo kwani usipojua namna ya kuitumia vizuri unaweza kuona ni gharama au inakwisha mapema kumbe anayetumia hajui jinsi ya kutumia hasa kufungua mtungi au jinsi ya kuufunga.

“Kwahiyo wananchi wakifika katika maduka yetu watapata elimu ya namna gani wanaweza kutumia nishati safi ya kupikia mitingi yetu.Mbali ya kupata elimu hiyo Oryx Gas tumekuja na utaratibu wa kupeleka huduma kwa wananchi kwani ukishanunua mtu hutaubeba bali utaacha namba ya simu na sisi tutakuletea mpaka ulipo kwa gharama zetu.

“Hivyo ili kuhakikisha wananchi wanapata nishati safi kwa wakati tunaendelea na kufunga maduka haya maalum ambako kwa nchi nzima yapo 1000 na tunaendelea kufungua mengine likiwemo hili la Banana kwa NASSCO na wiki iliyopita tumefungua duka Masenze.”

Kwa upande wake Tarik Nassoro ambaye ni Mkurugenzi wa NASSCO ambayo Wakala wa Oryx Gas amesema kwa kushirikiana na Oryx wamefungua maduka katika maeneo mengi wilayani Ilala huku akiwaomba Watanzania kuendelea kutumia gesi ya oryx na waache kutumia nishati ambazo zinachafua mazingira .

Wakati huo huo Baba Lishe Dickson Kuga na Mama Lishe Beatrice Shayo wametoa rai kwa mama na baba lishe nchini kutumia nishati safi ya kupikia katika kuandaa chakula kwani nishati safi inaokoa muda lakini pia haina madhara kiafya kama wakitumia kuni na mkaa.








Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir,akizungumza wakati akifunga Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo leo Aprili 30,2026 jijini Dodoma.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir,akizungumza wakati akifunga Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo leo Aprili 30,2026 jijini Dodoma.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir,akizungumza wakati akifunga Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo leo Aprili 30,2026 jijini Dodoma.

Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo,akizungumza wakati wa   Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo uliofanyika leo Aprili 29,2029 jijini Dodoma.

Sehemu ya washiriki wakisikiliza Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir (hayupo pichani) wakati akifunga Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo leo Aprili 30,2026 jijini Dodoma.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir,akiwa katika picha ya pamoja wakati akifunga Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo leo Aprili 30,2026 jijini Dodoma.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir,akiwa katika picha ya pamoja wakati akifunga Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo leo Aprili 30,2026 jijini Dodoma.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir,akiwa katika picha ya pamoja wakati akifunga Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo leo Aprili 30,2026 jijini Dodoma.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir,akiwa katika picha ya pamoja wakati akifunga Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo leo Aprili 30,2026 jijini Dodoma.

......

Serikali imewataka watumishi wa sekta ya elimu nchini kuimarisha mshikamano, uwajibikaji na ubunifu ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa elimu bora inayokidhi mahitaji ya karne ya 21.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir wakati akifunga Mkutano wa Pili wa Baraza la 37 la Wafanyakazi wa Wizara hiyo uliofanyika leo Aprili 30,2026 jijini Dodoma.

Mhe.Ameir  amesisitiza kuwa mafanikio ya sekta ya elimu yanategemea kwa kiasi kikubwa ushirikiano kati ya wafanyakazi, menejimenti pamoja na wadau wote wa elimu, akibainisha kuwa mshikamano huo ni chachu ya kuleta mageuzi chanya na endelevu.

Ametoa pongezi kwa uongozi wa Wizara, ukiongozwa na Waziri Adolf Mkenda, kwa kuendelea kusimamia mageuzi ya elimu ikiwemo maboresho ya sera na mitaala inayolenga kuendana na maendeleo ya sayansi na teknolojia duniani.

Aidha, amempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa uongozi wake unaoendelea kuleta mabadiliko makubwa katika sekta ya elimu, hususan katika kukuza ubora wa elimu, ubunifu na tafiti.

" Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuimarisha elimu, ikiwemo uzinduzi wa Mkakati wa Kisayansi wa Kuimarisha Stadi za Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK) pamoja na mpango wa kuunganisha taasisi za elimu na waajiri."amesema Mhe.Ameir

Ameeleza kuwa mipango hiyo inalenga kuwajengea wanafunzi ujuzi unaoendana na mahitaji ya soko la ajira na hivyo kuongeza ushindani wao kitaifa na kimataifa.

Hata hivyo amewataka wajumbe wa baraza hilo kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za utumishi wa umma, akisisitiza umuhimu wa kuwa na maadili, nidhamu na uwajibikaji kazini.

Amebainisha kuwa baraza la wafanyakazi limeendelea kuwa jukwaa muhimu la majadiliano, ushauri na maamuzi yanayochangia kuboresha utendaji kazi pamoja na ustawi wa watumishi.

Katika mkutano huo, mada mbalimbali zilijadiliwa ikiwemo bajeti ya wizara, usimamizi wa rasilimali watu, maadili ya utumishi wa umma na afya ya akili mahali pa kazi.

Ameir amesema  mada hizo zina mchango mkubwa katika kuboresha mazingira ya kazi na kuongeza tija kwa watumishi, hivyo kuimarisha utoaji wa huduma bora kwa wananchi.

Aidha Ameir ametoa wito kwa watumishi wote kuendelea kudumisha mshikamano, uzalendo na uadilifu, pamoja na kuwa mabalozi wa kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa elimu.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Prof.Carolyne Nombo, amesema kuwa utekelezaji wa kaulimbiu ya mkutano wa wafanyakazi ya “Ushirikishwaji na Mshikamano wa Wafanyakazi ni Chachu ya Kuimarisha Elimu Inayochochea Ubunifu” ni muhimu katika kufanikisha malengo ya sekta ya elimu nchini.

Prof. Nombo amesisitiza kuwa mshikamano na ushirikiano kazini ni msingi wa kuleta mabadiliko ya kweli katika sekta ya elimu.

Ameeleza kuwa kaulimbiu hiyo inalenga kuwajenga watumishi kuwa na utamaduni wa kufanya kazi kwa pamoja, kwa bidii na kwa uwajibikaji, hali ambayo itachochea mageuzi makubwa yanayohitajika katika kuboresha ubora wa elimu nchini.

“Tunaposhirikiana na kufanya kazi kwa bidii kama timu moja, tunaweka msingi imara wa kuleta mabadiliko chanya katika sekta ya elimu, yanayoakisi dira ya maendeleo ya taifa ya mwaka 2050,” amesema Prof. Nombo.

Ameongeza kuwa juhudi hizo zinapaswa kuendana na utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 (toleo la 2023), pamoja na kuzingatia mabadiliko mbalimbali yaliyofanyika katika mitaala iliyoboreshwa.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa watumishi kuzingatia sheria, kanuni, taratibu na miongozo ya serikali katika kutekeleza majukumu yao, akibainisha kuwa nidhamu na uwajibikaji ni nguzo muhimu za kufanikisha malengo ya wizara.





Na Oscar Assenga, Tanga

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Dkt. Balozi Batilda Burian, amesema mkoa huo umeanza mkakati maalum wa kukuza na kutangaza utalii wa fukwe pamoja na fursa za uwekezaji zilizopo, ili kuongeza mchango wake katika uchumi wa Taifa.

Akizungumza , amesema ameita wadau mbalimbali kwa ajili ya kujadili na kuweka mikakati ya pamoja ya kuitangaza Tanga, akibainisha kuwa mkoa huo umejaliwa kuwa katika ukanda wa Bahari ya Hindi wenye maeneo mengi yenye fursa za kiuchumi na utalii.

Ametaja baadhi ya maeneo hayo kuwa ni pamoja na Kipumbwi (Pangani), Ushongo, Kwale (Mkinga) na maeneo ya Raskazone jijini Tanga, ambapo kuna mradi wa kuboresha fukwe unaofadhiliwa na Benki ya Dunia.

Amesema mradi huo utakapokamilika utafungua fursa za michezo ya maji, matembezi ya boti, kuogelea pamoja na shughuli za kijamii kama harusi.


Aidha, amesema mkoa umeanza kushirikiana na Kampuni ya Makazi Solution pamoja na wadau wa Zanzibar ili kujifunza na kubadilishana uzoefu wa namna ya kuendeleza utalii wa fukwe.

Timu ya wataalamu inatarajiwa kwenda Zanzibar kukutana na Wizara ya Utalii na wadau wengine ili kuimarisha ushirikiano huo.

“Tunajifunza kutoka Zanzibar, ambako maeneo kama Nungwi na Paje yalianza kidogo lakini sasa yamekua vituo vikubwa vya utalii. Sasa ni wakati wa Tanga kuchukua nafasi hiyo,” amesema.

Kwa upande wa uwekezaji, Dkt. Burian ameeleza kuwa mradi wa Kipumbwi Satellite City, unaotekelezwa kwa ushirikiano na Halmashauri ya Pangani na Makazi Solution, unalenga kutoa fursa kwa wananchi na wawekezaji kupata viwanja na kuendeleza eneo hilo.


Amesema eneo la Kipumbwi lina umuhimu mkubwa kimkakati, likiwa kilomita 3 kutoka bandari ya Kipumbwi, kilomita 80 kutoka Tanga, kilomita 60 kutoka Zanzibar kwa njia ya bahari, na kilomita 180 kutoka Dar es Salaam. Pia ujenzi wa barabara ya Tanga–Pangani–Saadani–Bagamoyo unatarajiwa kufungua zaidi ukanda huo wa pwani.

Mbali na fukwe, mkoa wa Tanga una vivutio vingi vya utalii ikiwemo Mapango ya Amboni, Hifadhi ya Taifa ya Saadani, Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi, Milima ya Usambara (Lushoto), pamoja na urithi wa kihistoria kama makaburi ya vita ya kwanza ya dunia na Kisiwa cha Toten.

Ameongeza kuwa Tanga pia ni kitovu cha utamaduni wa Kiswahili, likiwa na historia ya muziki wa taarab, vyakula vya asili, pamoja na kuwa chimbuko la lugha ya Kiswahili, ambapo mwanazuoni mashuhuri Sheikh Shaban Robert alizaliwa katika eneo hilo.

Kwa sasa, amesema mkoa unapokea wageni kutoka ndani na nje ya nchi, hususan kutoka Kenya, Ujerumani, Uholanzi na Uswisi, wanaovutiwa na historia, mazingira asilia na utamaduni wa Tanga.

Dkt. Burian amesema jitihada hizo zinaunga mkono azma ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kuitangaza Tanzania kupitia kampeni ya Royal Tour na kuongeza idadi ya watalii.

Kwa upande wa uchumi, amesema mkoa wa Tanga kwa sasa unachangia takribani shilingi trilioni 9.8 katika pato la taifa, na una mpango wa kuongeza mchango huo na kufikia nafasi ya pili kitaifa baada ya Dar es Salaam ifikapo mwaka 2028.

Amehitimisha kwa kusema kuwa Tanga ni eneo sahihi kwa uwekezaji na utalii, akiwakaribisha wawekezaji na watalii kutoka ndani na nje ya nchi kuja kutumia fursa zilizopo.Kwa upande wake Afisa Mahusiano kutoka Kampuni ya Makazi Solution(T) Limited Maximilian Lukosi amesma dhamira yako kubwa ni kuufanya mkoa wa Tanga kuwa daraja la watalii ili wakitokea Zanzibar wapiti hapa na ndio waelekee mikoa mingine ikiwemo Kilimanjaro na Arusha

Top News