Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amekihakikishia Chama cha Mawakili Zanzibar kuwa Serikali inathamini na kuunga mkono kazi nzuri inayofanywa na taasisi hiyo ya kuwasaidia wananchi katika masuala ya kisheria.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 09 Aprili 2026, alipokutana na uongozi wa Chama cha Mawakili Zanzibar ulioongozwa na Rais wa chama hicho, Wakili Joseph Shaban Magazi, waliofika Ikulu, Zanzibar.

Hata hivyo, ameshauri uongozi wa chama hicho kulipatia ufumbuzi wa kudumu tatizo la wanafunzi wa ngazi ya digrii ya sheria wanaoshindwa kuendelea na masomo. 

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amepongeza uamuzi wa Chama cha Mawakili Afrika Mashariki kufanya mkutano mkuu wa mwaka hapa Zanzibar, na kwamba Serikali, kwa kushirikiana na wadau, itaunga mkono kufanikisha mkutano huo.

Naye Rais wa Chama cha Mawakili Zanzibar, Ndugu Joseph Shaban Magazi, amempongeza Rais Dkt. Mwinyi kwa uongozi wake na juhudi zake katika kuifungua Zanzibar na kuifanya kuwa kituo bora cha uwekezaji kwa nchi za Afrika Mashariki na Kati

Kwa upande mwingine,  Rais Dkt. Mwinyi ametumia fursa hiyo kuikabidhi gari taasisi hiyo, ambayo iliomba katika maadhimisho ya Siku ya Sheria yaliyopita, kwa ajili ya utekelezaji wa majukumu yake.











Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limetoa tuzo kwa washindi 10 wa shindano la insha la viwango la mwaka 2024/2025, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Viwango Afrika mwaka 2026. 

Washindi hao wametoka katika vyuo mbalimbali nchini, ambapo jumla ya washiriki walikuwa wanafunzi 522 wa elimu ya juu kati yao, wanawake walikuwa 230 na wanaume 292, huku shindano hilo likiratibiwa na Shirika la Viwango Afrika (ARSO).

Akizungumza leo Aprili 9, 2026 jijini Dar es Salaam katika hafla hiyo, Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Utekelezaji wa Sheria wa TBS, Dkt. Candida Shirima, akimwakilisha Mkurugenzi Mkuu, amesema taasisi hiyo inatambua mchango wa washiriki hao katika kuongeza uelewa wa viwango na kuelimisha jamii.

Amesema viwango vina mchango mkubwa katika kukuza biashara kwa kuongeza uaminifu kwa walaji, kuchochea biashara endelevu na kukuza uchumi wa taifa, huku akisisitiza umuhimu wa kuzingatia viwango kila siku.

Kwa upande wake, Jaji Mkuu wa shindano hilo, Dkt. Jalia Muna, amesema insha tano bora kutoka kwa washindi hao zitawasilishwa ARSO kwa ajili ya kushindanishwa barani Afrika, na maoni ya washindi yatasaidia kuboresha utendaji kazi wa TBS.
















Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Rhimo Nyansaho, tarehe 9 Aprili 2026 amekutana na kufanya mazungumzo ya kikazi na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Ulinzi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Guy Kabombo Muadiamvita, aliyekuwa katika ziara rasmi nchini Tanzania.


Mazungumzo hayo yamefanyika katika Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa, Kikombo jijini Dodoma, yakilenga kuimarisha ushirikiano wa kihistoria na kidiplomasia wa ulinzi kati ya Tanzania na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Katika kikao hicho, Dkt. Nyansaho alimhakikishia mgeni wake kuwa Serikali ya Tanzania, chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, iko tayari kuendeleza ushirikiano na DRC katika sekta mbalimbali za ulinzi. Maeneo hayo ni pamoja na kubadilishana wataalamu, kutoa mafunzo ya kijeshi, pamoja na kushirikiana kukabiliana na changamoto za kiusalama kama uhalifu wa mtandaoni na ugaidi.

Aidha, Dkt. Nyansaho alieleza kuwa ziara ya Mhe. Kabombo ni ishara ya uhusiano imara uliopo kati ya nchi hizo mbili, na inaonesha dhamira ya pamoja ya kuendeleza urafiki, maelewano na ushirikiano wa muda mrefu. Alisisitiza kuwa mazungumzo ya mara kwa mara yamekuwa msingi muhimu katika kujenga ushirikiano madhubuti kati ya Tanzania na DRC.

“Nina imani kuwa kupitia ushirikiano wetu, tutaweza si tu kukabiliana na changamoto za pamoja, bali pia kutumia fursa zilizopo kukuza uchumi na ustawi wa wananchi wetu,” alisema Dkt. Nyansaho.

Kwa upande mwingine, alibainisha kuwa ushirikiano wa kiuchumi kati ya Tanzania na DRC una nafasi kubwa ya kuimarika zaidi, hususan kupitia matumizi ya Bandari ya Dar es Salaam katika usafirishaji wa mizigo, jambo litakalochochea maendeleo ya pande zote mbili.

Mwisho, Waziri Nyansaho alisisitiza dhamira ya Tanzania kuona DRC inaimarika kiusalama na kiuchumi, akieleza kuwa mafanikio ya nchi moja ni faida kwa ukanda mzima.









Na: Dk. Reubeni Lumbagala

Nakumbuka mwalimu wangu wa somo la Uraia (Civics) alipokuwa akitufundisha mada (topic) ya "Haki za "Binadamu" (Human Rights) tulipokuwa Kidato cha Kwanza, alituambia mengi kuhusu haki za binadamu. 

Miongoni mwa mikazo yake, alituambia hivi: Haki ya kuishi (Right to life) ndiyo haki kubwa kuliko zote maana mtu anapokuwa hai ndipo anakuwa na uwezo wa kupata haki nyingine zote. Nilimwelewa vizuri sana.

Kimsingi, uhai ni muhimu katika maisha ya mwanadamu, ndiyo maana inapotokea mtu ameugua, na akawa hana uwezo wa kumudu gharama za matibabu yake, basi familia, ndugu, jamaa na marafiki hushikamana kwa kuchangishana fedha kunusuru uhai wa ndugu yao huyo.

Watoto ni kundi ambalo lipo hatarini kukabiliwa na magonjwa mbalimbali. Ni kutokana na msingi huo, serikali inajitahidi sana kutoa chanjo za magonjwa mbalimbali ili kuimarisha na kujenga afya zao ili kuwa na kinga ya kutosha ya kuweza kupambana na magonjwa.

Taasisi ya Doris Mollel (DMF) ni wadau muhimu hapa nchini katika suala la afya ya mama na watoto. Ni taasisi inayopambana sana kuhakikisha maisha ya mama na watoto yanakuwa salama dhidi ya vifo hasa vitokanavyo na uzazi.

Taasisi hii chini ya uongozi wa Mkurugenzi Mtendaji wake, Doris Mollel, imejikita katika kusaidia vifaa vya kuweza kuokoa maisha ya watoto wanaozaliwa kabla ya muhula (njiti) katika vituo vya afya na hospitali mbalimbali nchini.

Bi. Mollel alipata msukumo wa kuanzisha taasisi hii kwani yeye ni miongoni mwa watoto waliozaliwa kabla ya muhula na alizaliwa mama yake alipokuwa na ujauzito wenye wiki  27 huku akizaliwa na uzito wa gramu 900 tu. Kupona kwake kumempa msukumo wa kutetea maisha ya wanawake na watoto ili wawe salama katika suala zima la uzazi kwa  kuwezesha upatikanaji wa vifaa vya afya. 

Kupitia taasisi hii, vituo vya afya na hospitali nyingi zimepata msaada wa vifaa, jambo linalosaidia kuokoa maisha ya maelfu ya wanawake na watoto. Hata mtoto anapozaliwa na uzito pungufu, anapata wasaa wa kuwekewa kwenye wodi maalum ya uangalizi wa watoto njiti (NICU).

Aidha, kutokana na vifaa vilivyopo humo na unyonyeshaji unaoendelea kutoka kwa mama yake, uzito wa mtoto huongezeka. Na pale wataalamu wanapojiridhisha juu ya kuimarika kwa afya ya mtoto, mtoto huyo hutolewa katika wodi hiyo na kuendelea na maisha mengine ya kunyonya kutoka kwa mama yake.

Mwezi Machi, 2026, Shirika la Afya Duniani (WHO) limetambua kazi kubwa na nyingi zinazofanywa na DMF, na hivyo kumpa tuzo ya heshima Doris Mollel kama njia ya kutambua mchango wake katika kuboresha na kukuza afya mama na mtoto nchini Tanzania.

Tuzo hiyo ilitolewa na Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dk. Tedros Ghebreyesus katika Makao Makuu ya WHO, Geneva, Uswisi. Binafsi, nampongeza Bi. Mollel kwa tuzo hiyo kwani jitihada zake za kupigania afya ya mama na watoto zimezaa matunda, na maisha ya wengi yameokolewa kupitia juhudi zake. 

Harakati za Bi.Mollel zinaongozwa na kauli yake isemayo "Nikiacha kupigana, watoto njiti watafariki". Hakika, tuzo hii ni heshima kwa Bi.Mollel na Tanzania kwa ujumla.


Maoni; 0620 800 462



Na Said Mwishehe,Michuzi TV

UONGOZI wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Kilimanjaro Christian Medical Centre(KCMC) umewaomba Watanzania waliopo ndani na nje ya nchi kuchangia ujenzi wa jengo la matibabu ya moyo-KCMC ambapo kiasi cha Sh.bilioni 25 kinahitajika kukamilisha jengo hilo.

Akizungumza leo Aprili 9,2026 jijini Dar es Salaam Mkurugenzi Mtendaji wa KCMC Profesaa Gileard Masenga amesema ujenzi wa jengo hilo utagharimu Sh.bilioni 25 za kitandania na Vifaa tiba na vifaa vya hospitali vitagharimu jumla ya kiasi cha shilingi bilioni 25.

Aidha amesema amesema wataalamu watakaohudumia kitengo hicho tayari wameshapata mafunzo yao nchini India na Tanzania na wamepata ufadhiliwa kutoka kwa mdau aitwae Global Heartcare Foundation.

“KCMC tayari imeingia makubaliano ya ushirikiano na wadau wa kimataifa ambao wamekubali kufadhili asilimia 90 ya gharama za ujenzi.Hivyo tumekuja kwenu Watanzania kuomba mchangie asilimia 10 ya mchango wa ujenzi kwani tayari asilimia 90 ya fedha ya ujenzi ilishapatikana.”

Hivyo ametoa rai kwa watanzania wote (ndani na nje ya nchi) kuungana katika juhudi hiyo ya kitaifa kwani lengo ifikapo Julai mwaka 2027 huduma za matibabu ya moyo yawe yameanza kutolewa kuokoa maisha ya Watanzania wanaosumbuliwa na magonjwa ya moyo nchini.

“Huu si mradi wa KCMC pekee. Huu ni mradi wa Watanzania wote. Ni mradi wa kulinda maisha ya ndugu zetu, wazazi wetu, watoto wetu, na vizazi vijavyo.

“Tunawaomba Watanzania wa kila rika na kila nafasi vijana, wazee, wafanyabiashara, wafanyakazi, wakulima, viongozi, na diaspora yetu kuchangia kwa moyo wa uzalendo na mshikamano.Kila mchango ni muhimu. Kila mchango ni uhai. Kila mchango ni tumaini.”

Amesisitiza “Kwa pamoja, tunaweza kujenga kituo hiki.Kwa pamoja, tunaweza kuokoa maisha.Na kwa pamoja, tunaweza kuandika historia mpya ya huduma za afya chini Tanzania.”

Jinsi ya kuchagia Profesa Masenga amesema Watanzania wanaweza kuchangia kupitia njia zifuatazo: AKAUNTI JINA: KCMC MOYO

Bank of Africa - 04563580007

CRDB Bank - 0150686858800

NMB Bank - 40310194610

NBC Bank - 017172000770

MITANDAO YA SIMU:

Mixx by Yas - 15175376

Halotel (Halopesa) - 23758475


Aidha, kwa wale watakaopenda kutoa michango yao ana kwa ana, wanakaribishiwa kufika moja kwa moja katika hospitali ya KCMC huku akisisitiza kuwa jukumu la afya sio la Serikali tu. “Hiyo ndo maana KCMC inataka kuanza huduma hii.”

Amesema pia jengo hilo litakapokamilika litakuwa la kisasa lenye ghorofa tatu ambapo litakalojumuisha vyumba viwili vya upasuaji wa moyo (cardiac surgery theatre),maabara mbili za uchunguzi wa mishipa ya moyo (catheterization laboratory).

Pia vyumba vya wagonjwa mahututi (Intensive Care Unit - ICU) kwa watu wazima na watoto, Vitengo vya uangalizi maalum baada ya ICU (step-down ICU units),Vitanda 102 vya wagonjwa wa ndani,kliniki za wagonjwa wa nje, kitengo cha urekebishaji wa afya ya moyo (cardiac rehabilitation unit) na mabaara za uchunguzi na huduma za dawa.

Awali Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Watoto katika hospitali ya KCMC Dk.Ronald Mbwasi amesema kwa magonjwa ya moyo yasiyoambukiza kwa sasa yanachangia takribani asilimia 70 ya vifo duniani. Miongoni mwa magonjwa haya, magonjwa ya moyo na mishipa (cardiovascular diseases - CVDs) ndiyo chanzo kikuu cha vifo.

“Magonjwa kama Kiharusi (stroke) na Ugonjwa wa kuziba kwa mishipa ya moyo (ischemic heart disease) yanachangia sehemu kubwa ya vifo hivi. Zaidi ya asilimia 78 ya vifo vinavyotokana na magonjwa yasiyoambukiza hutokea katika nchi zenye kipato cha chini na cha kati (lower and middle income). 

“Magonjwa ya moyo ni miongoni mwa sababu kuu za wagonjwa kulazwa KCMC; takwimu za

hospitali zinaonyesha asilimia 14.4 ya wagonjwa wanaolazwa ni wagonjwa wa moyo ambapo hulazwa hospitalini kwa wastani wa siku 9 hadi 10…

“Na asilimia 38.5 ya wagonjwa wanaoruhusia hulazwa tena hospitalini baada ya muda na hivyo kiwango cha vifo kwa wagonj wa wa moyo ni takribani asilimia 18.3 ya vifo vyote vinavyotokea KCMC.”













Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe.Prof.Adolf Mkenda amesema Hafla ya Nne ya Tuzo ya Taifa ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu Inatarajia kufanyika tarehe 13 Aprili 2026 jijini Dar es Salaam katika ukumbi wa Super Dome Masaki. 

Mhe. Adolf Mkenda ameyasema hayo April 8, 2026 jijini Dodoma, Wakati akizungumza na Waandishi wa Habari amesema, hafla hii hufanyika kila mwaka kuadhimisha siku ya kuzaliwa kwa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere na kutambua mchango wake katika kukuza lugha ya Kiswahili na utamaduni wa Taifa. 

Ameeleza kuwa Mwaka huu, mashindano yamehusisha nyanja nne za fasihi riwaya, hadithi za watoto, tamthiliya na ushairi.

 "Tunaendelea kukuza kiswahili, kuendeleza vipaji vya uandishi bunifu, kulinda historia na utamaduni wa Taifa, pamoja na kuongeza hifadhi ya vitabu katika maktaba ndio malengo ya tuzo hii", amesema Prof. Mkenda.

 Sambamba na hayo Mhe. Adolf Mkenda amesema, Katika hafla hiyo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa mshairi maarufu duniani Abdilatif Abdallah, mwenye asili ya Afrika Mashariki, ambaye aliwahi kufundisha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa zaidi ya miaka 15. 

Hafla hiyo itatanguliwa na mjadala wa kitaaluma utakaoshirikisha waandishi bunifu wa Tanzania pamoja na wageni mashuhuri kutoka Uganda na Rwanda.




 

VICTOR MASANGU,KIBAHA .

Chama cha mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kibaha  mjini imewapongeza kwa dhati wanachama wake na wananchi kwa ujumla kwa kuweza kukipa kura nyingi za kishindo wakati  wa uchaguzi mkuu uliofanyika octoba 29 mwaka 2026.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa chama hicho Mwalimu Mwajuma Nyamka wakati wa ziara maalumu ambayo imeanza leo rasmi katika kata ya Mbwawa yenye lengo  kubwa la kuwashukuru wanachama pamoja na wanannchi.

Katika ziara hiyo ambayo imehudhuliwa na viongozi mbali mbali wa chama hicho pamoja na baadhi ya viongozi wa  jumuiya ya Wazazi,pamoja na jumuiya ya umoja wa wanawake wa (UWT) Kibaha mjini wameweza kuwatembelea  na kuzungumza na baadhi ya mabalozi wa matawi Kata ya Mbwawa.

Mwenyekiti Nyamka amesema kwamba pamoja na ziara hiyo kulenga kutoa shukrani pia ameanbatana na baadhi ya wataalamu kutoka Ofisi ya vizazi na vifo Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha (Rita) kwa  lengo la kuwasaidia wananchi wenye changamoto ya ukosefu wa vyeti vya kuzaliwa.

"Mimi kama mwenyekiti wa chama cha mapinduzi (CCM)  Wilaya ya Kibaha mjini pamoja na  viongozi wenzangu tumeanza ziara rasmi ya kuwashukuru wanachama pamoja na wananchi kwa ajili ya kutoa pongezi na shukrani kwa kukipigania chama kushi da  kwa kishindo katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2026,"amesema Mwenyekiti Nyamka.

Nyamka amebainisha kwamba   amefarijika sana na kitendo cha wanachama wa ccm sambamba na wananchi wote kuweza kupambana na kuchagua mafiga matatu kwa kishindo  katika nafasi ya udiwani,ubunge,pamoja na kiti cha Urais.

Kadhalika amewahimiza wanachama kuendelea kushikamana  kwa kishindo kuanzia ngazi za chini lengo ikiwa ni kuweza kukiimarisha chama ikiwa pamoja na kutekeleza ilani kwa vitendo.

Nao baadhi ya viongozi mbali mbali wa mashina wakizungumza kwa nyakati tofauti wamempongeza kwa dhati Mwenyekiti wa CCM Mwalimu Mwajuma Nyamka kwa kuweza kufanya ziara hiyo  na kwenda kuwatembelea na kuwajulia hali zao.

Mmoja wa balozi kutoka Mbwawa shule shina namba  nne Ramadhani Chuma alikishukuru chama chake kwa kuweza kuona umuhimu mkubwa wa kwenda nyumbani kwake kumtembelea kitendo ambacho kimeweza kumfariji sana.

ZIara ya Mwenyekiti wa Chama cha mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kibaha mjini Mwalimu Mwajuma Nyamka imeanza leo rasmi katika kata ya Mbwawa ambapo imetembelea baadhi ya viongozi wakiwemo mabalozi pamoja na kufanya mkutano wa hadhara kwa lengo la kuwashukuru wanachama na wananchi.





 


Top News