Na Mwandishi Wetu.

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imesisitiza kuwa uhuru wa vyombo vya habari nchini upo, unalindwa kisheria na unatambuliwa katika Katiba pamoja na Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, huku ikitoa wito kwa wanahabari kuzingatia maadili na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao.

Kauli hiyo ya JAB imetolewa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi hiyo, Wakili Patrick Kipangula, alipokuwa akizungumza katika kipindi cha moja kwa moja cha Hatua za Ushindi kinachorushwa na Kituo cha Televisheni cha Hope Channel Tanzania, leo Machi 17, 2026 jijini Dar es Salaam.

Ameeleza kuwa kifungu cha 7 cha Sheria ya Huduma za Habari kinaweka bayana haki na uhuru wa vyombo vya habari, ikiwa ni pamoja na haki ya mwandishi wa habari kutafuta, kuchakata na kusambaza taarifa, huku wananchi wakiwa na haki ya kupata taarifa sahihi kuhusu maendeleo yanayowazunguka.

“Uhuru wa vyombo vya habari upo na unalindwa kisheria. Mwandishi ana haki ya kutafuta na kusambaza taarifa, na mwananchi ana haki ya kupata taarifa. Huu ndio msingi wa uwazi na uwajibikaji katika jamii,” amesema Wakili Kipangula.

Hata hivyo, amesisitiza kuwa uhuru huo unaambatana na wajibu wa kuzingatia maadili ya taaluma, akibainisha kuwa dhana ya uwajibikaji haipaswi kuchanganywa na kile kinachoitwa ukandamizaji wa vyombo vya habari.

Amebainisha kuwa baadhi ya malalamiko ya ukandamizaji yanatokana na kutokuzingatia misingi ya kitaaluma, hususan pale ambapo taarifa zinapotolewa bila uthibitisho, uwiano au kwa lugha isiyozingatia maadili.

“Ni muhimu kutofautisha kati ya uwajibikaji na ukandamizaji. Usipozingatia maadili ya taaluma, usiseme unakandamizwa. Uwajibikaji ni sehemu ya taaluma, na haupaswi kutafsiriwa kama kubanwa kwa uhuru wa habari,” amesisitiza Kipangula.

Katika hatua nyingine, Wakili Kipangula ameeleza kuwa Serikali imeendelea kuboresha mazingira ya sekta ya habari kupitia mageuzi ya kisheria na kisera, ikiwemo kufutwa kwa Sheria ya Magazeti iliyokuwa ikitajwa kuwa kandamizi na kuanzishwa kwa Sheria ya Huduma za Habari inayolenga kuimarisha uhuru, uwajibikaji na weledi katika tasnia hiyo.

Amesema maboresho hayo yameleta mwelekeo mpya unaowezesha vyombo vya habari na wanahabari kufanya kazi zao kwa uhuru zaidi, huku wakizingatia viwango vinavyokubalika kitaaluma na kisheria.

Aidha, ametoa wito kwa wanahabari kuendelea kuilinda taaluma yao kwa kuzingatia ukweli, usahihi na uwiano katika utoaji wa taarifa, sambamba na kuheshimu haki za wananchi za kupata taarifa sahihi na kwa wakati kwa mujibu wa Sheria ya Kupata Taarifa.

Amesisitiza umuhimu kwa waajiri kote nchini kuhakikisha wanapata wataalamu wenye sifa stahiki kuingia katika menejimenti zao, sanjari na kuwatumia waandishi wenye ithibati, katika kazi zote za kihabari ili kulinda na kuipa thamani taaluma ya uandishi wa habari.

Na Mwandishi wetu

Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) limewataarifu wananchi wanaotumia usafiri kwa njia ya maji kutumia vyombo vya usafiri majini vilivyoidhinishwa kubeba abiria na kuepuka kupanda vyombo vya mizigo ambavyo haviruhusiwi kubeba abiria.

Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa na TASAC, wananchi wanahimizwa kuchukua tahadhari kufuatia visa vinavyoripotiwa vya baadhi ya wananchi kupanda vyombo vya mizigo kinyume cha sheria, jambo linaloongeza hatari ya ajali na kuathiri usalama wa maisha.

TASAC imeeleza kuwa vyombo vya mizigo havijaundwa wala kuidhinishwa kwa kubeba abiria, hivyo kuvitumia kinyume na masharti kunazidisha hatari, hasa wakati wa hali mbaya ya hewa au safari za usiku.

Taarifa hiyo imehimiza kuwa kila chombo cha usafiri majini kinapaswa kutumika kwa madhumuni yake yaliyoidhinishwa kisheria. Wamiliki na waendeshaji wanatakiwa kuzingatia kanuni za usalama ili kulinda maisha ya abiria na mali zao.

TASAC pia imewataka wananchi kuhakikisha wanapanda vyombo vinavyotambulika rasmi, vilivyo na vifaa vya usalama ikiwemo majaketi okozi, na vinazingatia idadi halali ya abiria. Aidha, TASAC imeonya kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya wamiliki au waendeshaji watakaokiuka sheria kwa kubeba abiria kwenye vyombo vya mizigo au kuvuka idadi halali ya abiria.

TASAC inaendelea kutoa wito kwa wananchi kushirikiana na mamlaka husika katika kuhakikisha usalama wa usafiri majini unazingatiwa kwa kufuata sheria na taratibu zilizowekwa.

Na Mwandishi Wetu

NAIBU Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Dkt. Mohammed Said Mohammed (DIMWA), amewahimiza viongozi na wanachama wa Chama hicho kuendelea kudumisha amani na utulivu nchini, sambamba na kushiriki kikamilifu katika kukijenga na kukiimarisha chama.

Ametoa mwito huo alipokuwa akizungumza katika hafla ya futari ya pamoja aliyoiandaa katika Ofisi Kuu ya CCM Kisiwandui Zanzibar, iliyohudhuriwa na viongozi, wanachama pamoja na wageni waalikwa, ikiwa ni sehemu ya kuendeleza mshikamano na kuimarisha mahusiano ndani yaCCM Zanzibar.

Akizungumza wakati wa futari hiyo Dkt. Dimwa amesisitiza kuwa mshikamano na nidhamu ndani ya chama ni nguzo muhimu katika kufanikisha malengo ya kisiasa na maendeleo ya taifa.

Ameongeza katika kipindi hiki, ni wajibu wa kila mwanachama ni kuhakikisha anakuwa balozi mzuri wa amani, hasa kwa kuzingatia kuwa CCM imejijengea sifa ya kuongoza kwa misingi ya utulivu na mshikamano wa kitaifa.

Dk.Dimwa amewataka pia  viongozi kuendelea kuwa karibu na wananchi, kusikiliza changamoto zao na kuzitafutia ufumbuzi kwa wakati ili kuimarisha imani ya wananchi kwa chama hicho.














Na. Jacob Kasiri - Serengeti

Kauli ya Hifadhi ya Taifa Serengeti kuwa ni darasa katika shughuli za ulinzi wa maliasili na eneo maarufu duniani kwa ajili ya utalii endelevu imeendelea kukita mizizi katika hifadhi hiyo iliyobeba umaarufu duniani kwa uhamaji wa nyumbu imedhihirika leo machi 17, 2026 baada ya kupokea Ujumbe Maalumu wa Wizara ya Utalii, Idara ya Hifadhi za Taifa na Wanyamapori (DPNW) ya Serikali ya Zambia.

Ujumbe huo ulioongozwa na Naibu Katibu Mkuu wa Baraza la Mawaziri Mhe. Siazongo Siakalenge ambaye pia anashughulikia masuala ya Fedha na Maendeleo ya Uchumi - Zambia alisema Hifadhi ya Taifa Serengeti ndio eneo sahihi kwao kujifunza namna uhifadhi na utalii ulivyoimarishwa na kuchangia kwa kiasi kikubwa uchumi wa Tanzania.

Aidha, Mhe. Siakalenge aliongeza; “Licha ya mabadiliko ya tabianchi yanavyoathiri kwa kiasi kikubwa Hifadhi za Taifa Duniani na Zambia ikiwa ni miongoni mwao lakini Hifadhi     ya Taifa Serengeti imeendelea kushamiri, tumeona wanyama wa kila aina, mimea na majani yamestawi huku maji yakiwa ya kutosha. Haya na mengine mengi tuliojifunza kwenu yametufungua macho na tunaenda kuyafanyia kazi.”

“Shughuli za utalii zinazofanyika Serengeti nyingi zinafanana na za Zambia isipokuwa utalii wa Puto (baloon) huu hatuna na katika ziara hii nimeuona na kuuonja, hivyo nasi tunaenda kuuanzisha pia”, alidadavua Mhe. Siakalenge.

Naye, Katibu Mkuu Wizara ya Utalii - Zambia Bw. Evans Muhanga alisema kuwa licha ya wasilisho zuri lilionesha ongezeko la watalii na mapato kwa Taifa, pia wamejionea watalii wengi katika maeneo mbalimbali ya vivutio walivyotembelea leo ikiwemo utalii wa puto ambapo zaidi ya puto 6 zilionekana zikielea angani zikiwa zimejaza watalii.

Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi Ismail Omary ambaye ni Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Serengeti alisema kuwa Ujumbe huo Maalumu kutoka serikali ya Zambia umeridhishwa na mikakati na mbinu mbalimbali za uhifadhi na utalii tulizoziwasilisha kwao zilizopelekea hifadhi hiyo kunyakua tuzo mbalimbali za kimataifa.

Aidha, Kamishna Ismail aliongeza kuwa hifadhi hiyo inajivunia kuwa na wanyama wakubwa watano (The Big 5) ikihusisha tembo, nyati, faru, simba na chui huku akisisitiza kuwa kwa mwaka 1993 hifadhi hiyo ilikuwa na faru weusi watatu tu lakini hadi 2025 hifadhi hiyo inajivunia kuwa na faru weusi zaidi ya 100.

Kabla ya wasilisho hilo, wajumbe hao  maalumu kutoka serikali ya Zambia walifanya utalii wa puto asubuhi na kujionea wanyama kutokea juu baadae walizuru maeneo mengine ya vivutio vya utalii likiwemo eneo la ndutu walipo nyumbu kwa sasa na kujionea nyumbu wakiwa na ndama lukuki.













Serikali imedhamiria kuwa Kampasi ya Mloganzila ya Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) itakuwa mji wa kitaaluma na tiba, ikijumuisha vituo vya umahiri vitakavyotoa huduma za matibabu, elimu na utafiti ili kuimarisha sekta ya afya na elimu ya juu nchini.

Hatua hiyo, inatokana na uwekezaji mkubwa unaoendelea katika Kampasi hiyo, pamoja na uwepo wa kituo cha umahiri cha magonjwa ya moyo na mishipa ya damu ambacho ni cha Kipekee Afrika Mashariki.

Ameongeza kuwa Serikali  imetenga dola za Marekani milioni 83 kwa ajili ya kujenga hospitali ya  tiba ya magonjwa hayo ikiwa ni sehemu ya Kituo hicho ili kuwezesha kufanya utafiti kutoa mafunzo kwa vitendo na pia huduma kwa wagonjwa.


 Aidha, Serikali imekamilisha mkakati wa kuanzisha kituo cha  umahiri cha tiba ya kinywa na meno cha  Afrika Mashariki .

Akizungumza Machi 17,2026 jijini Dar es Salaam katika ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, ameeleza kuwa, juhudi hizo zinatokana na maono ya Mhe. Rais kuifanya Tanzania kuwa kitovu na taaluma za tiba katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati na pia  kuhakikisha kama Taifa linazalisha wataalamu na wabobezi wa kutosha kuhudumia watanzania wageni kutoka nje wanaokuja kupata huduma.

‘‘’Lengo ni kufanya Kampasi ya Mloganzila kuwa na vituo vingi vya umahiri katika nyanja mbalimbali za tiba na tofauti ya vituo hivi na hospitali ni kwamba, vitafanya utafiti, mafunzo na kutoa huduma ya tiba, ” Amesema Waziri Mkenda. 

Prof. Mkenda ameongeza kuwa, Serikali pia inapanga kuanzisha kituo cha umahiri cha matibabu ya saratani ili kupanua wigo wa huduma za kibingwa nchini.

Kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET) kampasi ya Mloganzila imepatiwa zaidi ya shilingi bilioni 77 kwa ajili ya ujenzi wa Jengo la Utawala Ndaki ya Tiba, Jengo la TEHAMA na Maktaba, maabara, kumbi za mihadhara, jengo la Anatomia na hosteli ya wanawafunzi ambapo kwa ujimla kampasi hiyo  itachukua wanafunzi zaidi ya 1000.




 


Na Mwandishi Wetu, Michuzi TV
SHIRIKA la INADES-Formation Tanzania limezindua ujenzi wa bwawa la kunyweshea mifugo (water trough) katika Kijiji cha Migori, Wilaya ya Iringa, kwa lengo la kuboresha upatikanaji wa maji salama na ya uhakika kwa punda na mifugo mingine midogo.

Mradi huo unatekelezwa kwa ushirikiano na Brooke East Africa, kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Iringa pamoja na jamii ya Kijiji cha Migori.

Akizungumza wakati wa makabidhiano ya eneo la mradi, Diwani wa Migori ambaye ndio alikuwa mgeni rasmi, Fatma Moge, ameipongeza hatua hiyo akisema itasaidia kupunguza vifo visivyo vya lazima vya punda na mifugo mingine, hasa wakati wa kiangazi.

Ameeleza kuwa kata hiyo, inayojumuisha vijiji vitano, hukumbwa na uhaba mkubwa wa maji na malisho wakati wa vipindi vya ukame. Hali hiyo husababisha mifugo kupelekwa umbali mrefu kutafuta malisho, ambapo mara nyingi maji hayapatikani kwa urahisi.

Fatma pia ameitaka mamlaka ya wilaya kuendelea kutafuta ushirikiano zaidi ili kupanua ujenzi wa mabwawa ya kunyweshea mifugo katika vijiji vingine vinavyokabiliwa na changamoto kama hizo.

Kwa upande wake, Afisa Mifugo wa Wilaya ya Iringa, Isidori Karia, ambaye pia ni mratibu wa mradi wa ustawi wa punda na uboreshaji wa maisha ya jamii, amesema mradi huo tayari umechangia kuboresha maisha ya wananchi kupitia utunzaji bora wa punda.

Amesisitiza kuwa bwawa hilo jipya litanufaisha si punda pekee bali pia mifugo mingine katika eneo hilo.

Naye Dkt. Charles Bukula, daktari wa mifugo kutoka INADES-Formation Tanzania, ameeleza kuwa Kijiji cha Migori kilichaguliwa kutokana na changamoto kubwa zinazowakabili mifugo wakati wa kiangazi pamoja na idadi kubwa ya mifugo iliyopo eneo hilo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa wafugaji wa kijiji hicho, Sokoine Seketu, aliukaribisha mradi huo akisema umefika wakati muafaka na utasaidia si Migori pekee bali pia jamii za jirani.

Tangu mwaka 2019, INADES-Formation Tanzania imekuwa ikitekeleza mradi wa “Kusaidia maisha ya jamii kupitia uendelezaji wa ustawi wa punda” katika mikoa ya Singida, Iringa na Dodoma.

Mradi huo unalenga kuboresha maisha ya jamii, hasa makundi yaliyo hatarini yanayotegemea punda kwa kipato. Unajikita katika kuimarisha afya, uzalishaji na ustawi wa punda kupitia juhudi zinazoongozwa na jamii, ikiwemo matumizi sahihi ya vifaa vya kufungia (harness), huduma za mifugo, na elimu ya ufugaji bora.
Fatma Moge, Diwani wa Kata ya Migori (aliyevaa kofia), ambaye alikuwa mgeni rasmi wakati wa hafla ya makabidhiano ya eneo la ujenzi wa bwawa la kunyweshea mifugo kijijini humo, akipatiwa maelezo kuhusu mradi huo.
Jamii ya Migori, inayoundwa kwa kiasi kikubwa na wafugaji, wakikusanya na kupeleka vifaa vya ujenzi katika eneo la mradi.

Na Karama Kenyunko Michuzi Tv

KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo imeridhishwa na maendeleo ya mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET) ambao umefikia asilimia 70.

Akizungumza leo wakati wa ziara ya kutembelea Kampasi ya Mlonganzila, Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Husna Sekiboko alisema lengo la mradi huo ni kuongeza miundombinu na upanuzi wa Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (Muhas) kiweze kukua kama inavyotarajiwa.

Sekiboko alisema utekelezaji wa mradi wa HEET umepita matarajio yaliyopangwa katika mkataba kwani kuna maeneo utekelezaji umefikia asilimia 70 hadi 80.

"Mradi huu utaleta tija kwa Taifa kwani udahili utaongezeka, maeneo ya kujifunzia yataongezeka kwani bado kuna hekari nyingi," alisema

Aliongeza kuwa kutokana na ongezeko la watu, uwiano kati ya daktari na mgonjwa uko chini hivyo wakipanua vyuo vinavyohusika na kuandaa madaktari ili kupunguza uhaba wa madaktari na kuwa na nafasi nzuri ya kutoa huduma bora.

"Tunamshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa ushirikiano nzuri na Benki ya Dunia kwani imeweka katika mradi huu zaidi ya Shilingi bilioni 115 ambazo zinafanya upanuzi wa kampasi hii na maana yake ana makusudi ya kuongeza tija katika sekta ya afya," alieleza

Kwa upande wake, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda alisema eneo la Mlonganzila litakuwa eneo maalum la tiba kwani wanatarajia kujenga Hospitali maalum kwa ajili ya tafiti, kujifunzia na kufundishia za tiba ya kinywa na meno, magonjwa ya moyo na saratani.

Alisema wanaenda kuwa kituo cha umahiri Afrika Mashariki ambapo watachochea utalii tiba kwa kupokea wagonjwa kutoka nje ya nchi pamoja na wanafunzi watakaosomea ubobezi na umahiri katika fani mbalimbali kutoka nchi za nje.

Kaimu Makamu Mkuu wa chuo hicho, Profesa Balandya alisema jinsi wanavyoongeza kampasi wanavutia wawekezaji wa kutengeneza viwanda vya dawa.

"Mradi utakuwa na tija kwani kwa sasa wanaoomba kozi ya udaktari ni 5,400 na wote wanavigezo lakini wanaowachukua ni 230 pekee hivyo wanawaacha wengine," alisema.

Aliongeza "Wataalamu wanawatengeneza wenyewe Kwa mujibu wa vigezo vya Taasisi Vyuo Vikuu (TCU) wanaelekeza uwiano kati ya wanafunzi na walimu ni wanafunzi 10 kwa mwalimu moja na chuo hicho uwiano ni 11:1 hivyo wakiongeza udahili wanahitaji kuongeza walimu."










Na Diana Byera, Bukoba

MBUNGE wa Jimbo la Bukoba Mjini Mhandisi Johnstone Mtasingwa kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo wamefanikisha kununua mashine ya kudurufu mitihani katika Shule ya Msingi Bunena iliyoko Manispaa ya Bukoba baada ya zoezi hilo kukwama miaka mitano iliyopita.

Wadau wengine walioshiriana na Mbunge Mtasingwa ni Diwani wa kata Bakoba Shabani Rashidi, wazazi na walezi wa wanafunzi wa shule ya Msingi Bunena Manispaa ya Bukoba

Wanafunzi, Wazazi, walezi na uongozi wa shule wamepokea mashine hiyo ya kudurufu mitihani (Photocopy mashine) yenye thamani ya Shilingi 3,400,000 na kutoa pongezi kwa wadau wa maendeleo akiwemo Mbunge wa Jimbo la Bukoba Mjini ambaye alipokea kilio hicho wakati wa kampeini zake za kugombea ubunge na sasa anaendelea kushirikiana na wadau kutimiza haadi zake

Akizungumza kwa niaba ya Mbunge huyo wakati wa kukabidhi mashine hiyo Katibu wa Mbunge Hamada Simba amesema pia amepokea maombi ya kompyuta mbili za kuchapisha mitihani katika shule hiyo ambapo amesema atanunua kompyuta hizo haraka.

Amesema kuwa lengo ni kufanya wanafunzi wa shule hiyo kuzoea mitihani iliyochapishwa na kupunguza adha kwa wazazi na walezi wa wanafunzi

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Bakoba Shaban Rashid ametoa pongezi kwa ushirikiano kati ya ofisi ya Kata na ofisi ya Mbunge wa Jimbo kuhusu changamoto mbalimbali ambazo amezitatua kwa miezi mitano tangu amechaguliwa na kwamba Mbunge huyo amekuwa akijituma na anawafikia wananchi Haraka.

“Wananchi waendelee kumpa ushirikiano katika utendaji wa kazi na hadi kufikia miaka mitano watakuwa wamepata manufaa makubwa kupitia utendaji kazi wa Mbunge huyo.”

Awali Mwalimu Muu wa Shule ya msingi Bunena Devotha Mugisha amesema imewachukua wazazi miaka mitano kuchangia mashine hiyo lakini baada ya Kuona mwitikio wao Mbunge na diwani wameunga mkono jitihada zao.

Ambapo ametoa shukuran kwa viongozi hao na kuhaidi watoto watakaomaliza Darasa la Saba mwaka huu wengi wao watachaguliwa katika shule za vipaji maalumu.

Amesema shule hiyo ni miongoni mwa shule Kongwe ambayo ilianza mwaka 1902 na changamoto kubwa kwa sasa ilikuwa vifaa vya tehama jambo ambalo limetatuliwa.

Aidha amesema Serikali ya awamu ya Sita imekarabati shule hiyo ambayo hapo mwanzo ilijengwa kwa udongo na sasa inamazingira mazuri ya watoto kujifunzia.







Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amemwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kumbukizi ya miaka mitano ya kifo cha aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, iliyofanyika Kilimani, Chato mkoani Geita.

Akitoa salamu za Serikali, Makamu wa Rais amesema ili kumuezi Hayati Magufuli kwa vitendo ni vema kila Mtanzania kujifunza wito kwa kujitoa na kufanya kazi kwa bidii. Amesema Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, aliyejitambulisha kwa Falsafa yake ya “Hapa Kazi tu”, alitaka kila mtu kujituma na kutoa mchango wake kwa Taifa kwa njia ya kazi. Aliamini kuwa hiyo ndiyo njia pekee inayoweza kuondoa umaskini, katika ngazi ya mtu mmoja mmoja, kaya na hata Taifa kwa ujumla.

Makamu wa Rais amesema katika uongozi, funzo kutoka kwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli ni ujasiri na uthubutu wake katika kufanya maamuzi magumu na yenye manufaa kwa Taifa. Ameongeza kwamba alifundisha umuhimu wa kuwajibika na kusimamia misingi ya haki na usawa katika kuwahudumia wananchi wote, pia hakuyumbishwa katika kupiga vita uzembe na rushwa.

Halidhalika, Makamu wa Rais ameongeza kwamba, Hayati Magufuli, alifundisha kuwa hatima ya Tanzania na Afrika kwa ujumla iko mikononi mwa Watanzania na Waafrika wenyewe. Akisisitiza ulinzi na matumizi ya utajiri mkubwa wa rasilimali zilizopo, kwani zinaweza kuwatoa wananchi katika umaskini. Amesema, Hayati Magufuli aliamini kuwa wajibu wa kutatua matatizo ya nchi ya kijamii, kisiasa au kiuchumi yako mikononi mwa Watanzania wenyewe.

Makamu wa Rais amesema katika uhai wake, Hayati Dkt. John Magufuli aliwagusa wengi kupitia utumishi na uongozi wake uliotukuka. Pamoja na mambo mengine, Mwenyezi Mungu alimjalia Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, kipawa cha uongozi na uwezo mkubwa wa kunena na kutenda yote aliyoyaamini kuwa ya manufaa kwa Taifa na watu wake. Kila siku ya maisha yake ilijaa mafunzo kwa kila aliyemwona au kufanya naye kazi. Ameongeza kwamba, maisha yake yalikuwa ni darasa zuri kwa viongozi, na kupitia uongozi wake aliweza kulea na kuinua viongozi wapya wengi, hasa vijana.

Makamu wa Rais amesema, Rais Dkt. Samia Suhulu Hassan anaungana na Watanzania wote katika kumbukizi hiyo na Serikali anayoiongoza itaendelea kumuenzi Hayati Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuendeleza urathi wake.

Amesema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kutambua na kuenzi mchango wa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, amekuwa akifuatilia kwa karibu ujenzi wa makumbusho yake iliyopo Chato na kuamua kutoa shilingi milioni 100 zilizobaki ili kukamilisha ujenzi huo.

Kumbukizi hiyo imehudhuriwa na Rais wa Zanzibar Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi ambaye amesema, namna bora katika kumuenzi Hayati Magufuli ni kuendeleza dhamira yake ya kuhimiza uwajibikaji na kuwajali wananchi hususani wanyonge na kuhakikisha rasilimali za nchi zinalindwa kwa maslahi ya Watanzania wote.

Amesema Hayati Magufuli alikuwa muumini mkubwa wa Muungano wa Tanzania kwa kuhakikisha wananchi wa pande zote mbili wananufaika na Muungano huo. Amesema alisimamia vema uwajibikaji na mapambano dhidi ya ufisadi na wizi wa mali za umma hatua iliyochangia kwa kiasi kikubwa katika kuimarika kwa nidhamu katika utumishi wa umma na kulinda rasilimali za umma.

Ameupongeza uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jitihada za kusimamia, kuendeleza na kuhakikisha maono na malengo ya Hayati Magufuli yanatimizwa kwa vitendo.

Rais Dkt. Mwinyi, ametoa wito kwa Watanzania kumuenzi Hayati. Magufuli kwa kuendelea kutekeleza azma yake ya kudumisha tunu ya amani ili iendelee kuwa msingi wa mafanikio kiuchumi na kijamii. Vilevile amewahimiza Viongozi wa Dini, kuendelea kuliombea Taifa amani.

Akizungumza kwa niaba ya familia ya Hayati Dkt. John Magufuli, Mbunge wa Viti Maalum Mhe. Jesca Magufuli, amesema kama familia katika kumbukumbu za Hayati Dkt. Magufuli, wanamkumbuka kama mmoja ya Viongozi aliyobeba kwa uzito mkubwa jukumu la kuimarisha misingi ya maendeleo ya Taifa.

Ameishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna inavyoendelea kuhifadhi kumbukumbu za Hayati Dkt. Magufuli kwa heshima na staha inayostahili.

Aidha familia imempongeza na kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa ushirikiano aliyoutoa kwa familia katika kipindi chote cha miaka mitano pamoja na kuendeleza kazi za Hayati Dkt. Magufuli za ujenzi wa Taifa kwa kutambua kwamba historia ya Taifa lolote hujengwa na vizazi vilivyopokea wajibu kutoka kwa waliotangulia na kuendeleza safari ya maendeleo.

Katika Kumbukizi hiyo, jumla ya kiasi cha shilingi milioni 474 ikiwemo ahadi na fedha taslimu zimekusanywa katika harambee iliyoongozwa na Makamu wa Rais Dkt. Emmanuel Nchimbi kwa lengo la kumalizia ujenzi wa Kanisa Katoliki Parokia ya Kilimani Wilayani Chato.










Top News