Maafisa Ushirika wa vyama vya ushirika nchini wametakiwa kutumia ipasavyo elimu na maarifa waliyoyapata katika mafunzo maalum ili kuwa chachu ya mafanikio, uwajibikaji na maendeleo endelevu ndani ya vyama vya ushirika.

Akifunga rasmi mafunzo ya wiki mbili ya kuwajengea uwezo maafisa hao katika masuala ya usimamizi wa vyama, Mrajisi Msaidizi anayeshughulikia Uhamasishaji, Masoko na Uwekezaji amesema mafunzo hayo yamekuwa nyenzo muhimu katika kuimarisha ufanisi wa vyama vya ushirika, hususan katika ngazi za mikoa na kusisitiza kuwa mafunzo hayo yamewapa washiriki mbinu za kisasa za uongozi, usimamizi na ushirikishaji wanachama, hatua itakayosaidia kuongeza tija, uwazi na ushindani katika soko.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Isaiah Kapakala, alisema mafunzo hayo yalilenga pia kuwajengea washiriki uelewa mpana juu ya matumizi sahihi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), akibainisha kuwa matumizi ya teknolojia ni nguzo muhimu katika kuongeza ufanisi na uwajibikaji wa taasisi za ushirika katika zama za sasa.

Naye mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo, Sophia Kagimbo, amesema mafunzo hayo yamewapa msukumo mpya wa kufanya kazi kwa ubunifu, weledi na kujituma zaidi, akiahidi kuwa watatumia maarifa waliyoyapata kuhakikisha vyama vya ushirika vinapiga hatua kubwa za maendeleo kote nchini.

Mafunzo hayo ni sehemu ya mkakati wa kuimarisha sekta ya ushirika nchini ili iwe injini ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii.






Na Diana Byera,Kyerwa

MKUU wa Wilaya ya Kyerwa mkoani Kagera Zaituni Msofe, amekabidhi rasmi nyumba kwa familia ya Jenifer Richard mwenye uhitaji maalum Mkazi wa Kakerere katika Kata ya Nkwenda iliyojengwa.

Nyumba hiyo imejengwa na Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Kagera, Devotha Daniel Mburarugaba ikiwa ni sehemu ya juhudi zake za kusaidia wananchi wenye uhitaji maalum.

Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano, Msofe amemshukuru Mbunge kwa kugusa maisha ya wananchi kwa vitendo, akielez hatua hiyo ni mfano wa kuigwa katika kuimarisha mshikamano na utu kwa jamii.

“Ninawapongeza viongozi wanaotumia nafasi zao kuleta matumaini kwa wananchi. Nawahimiza watu wote wenye uwezo kujitokeza kuwasaidia wasiojiweza katika jamii yetu,” amesema Mkuu wa Wilaya Msofe.

Kwa upande wake, Mbunge Devotha Daniel Mburarugaba amesema aliguswa kuanza ujenzi wa nyumba hiyo baada ya kuona picha Mjongeo kupitia mitandao ya kijamii akiwa katika mazingira magumu ya maisha.

“Nilipoona hali aliyokuwa nayo, niliguswa na nikachukua hatua ya haraka. Leo tunashuhudia matokeo ya mshikamano na upendo,” amesema Mbunge huyo.

Aidha, Mbunge ameahidi pamoja na ujenzi wa nyumba hiyo, atahakikisha anakata bima ya afya kwa wote kwa familia yote ili kuwawezesha kupata huduma za matibabu kwa uhakika na kwa wakati.

Hata hivyo Mbunge Devotha Mburarugaba pia amempongeza Raisa Dk.Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuweka mazingira mazuri yanayowezesha viongozi kuwahudumia wananchi na kusimamia maendeleo ya watu wenye mahitaji maalum.

Kwa niaba ya familia, ndugu wa karibu wametoa shukrani za dhati kwa Mbunge na uongozi wa Wilaya ya Kyerwa kwa msaada huo mkubwa ambapo wamefafanua walikuwa wanaishi katika mazingira magumu kwa muda mrefu.

Hivyo nyumba hiyo ni mwanzo mpya wa maisha yao na imewarejeshea matumaini na heshima katika jamii. Walimuombea Mbunge na viongozi wote waliohusika baraka na mafanikio katika kuendelea kuwahudumia wananchi.







MKUU wa Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga Peter Masindi, amesema kulipa kodi ni muhimu sana kwa maendeleo ya Taifa kwani kupitia Kodi Serikali imeendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika jamii.

Ameyasema hayo hivi karibuni wakati alipotembelewa na Maafisa wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Ofisini kwake Wilayani Kishapu kwa lengo la kumjuulisha juu ya uwepo wa zoezi la elimu ya kodi mlango kwa mlango wilayani humo.

Masindi, amesema kupitia kodi Serikali imeendelea kuimarisha miundombinu mbalimbali na hatimae kuboresha huduma za kijamii.

"Ukilipa kodi ndio unajenga barabara, shule, hospitali, unachangia uwepo wa huduma za maji na miradi ya kimkakati kama Treni ya Mwendokasi (SGR)" amesema Masindi.

Aidha, ameipongeza TRA kwa kuendelea kukusanya kodi kwa mafanikio huku akitolea mfano wa kuvunja kwa rekodi ya makusanyo kwa kila mwezi kwa TRA Shinyanga na maeneo mbalimbali nchini Tanzania.

Mbali na hayo, amewapongeza wafanyabiashara wa Kishapu kwa kuendelea kulipa kodi kwa hiari huku akisisitiza TRA kuendelea na urasimishaji wa Wafanyabiashara kwani utaongeza wingi wa mapato na hatimae kuboresha huduma za kijamii kadri zinavyohitajika.

Pamoja na hayo, ameiomba TRA kuweka Ofisi ya Huduma za Kikodi Wilayani Kishapu kwani kukosekana kwa Ofisi katika Wilaya hiyo kunasababisha changamoto kwa walipakodi.

"Tunahitaji Ofisi ifunguliwe (Kishapu) kwa ajili ya kuwarahisishia walipakodi kuendelea kulipa kodi kwa hiari, kwani kwa sasa wananchi wanatembea umbali mrefu kwa ajili ya kuzifuata huduma za kikodi" amesema Mhe. Masindi.

Kwa Upande wake, Afisa Msimamizi wa Kodi mkoa wa Shinyanga Semeni Mbegi kwa niaba ya Kiongozi wa timu hiyo amesema katika kipindi cha takriban wiki moja wameweza kutembelea zaidi ya wafanyabiashara 2000 kwa kuwapatia elimu na kusikilza changamoto zao.

Amefafanua kuwa katika zoezi hilo wamebaini mambo mbalimbali ikiwemo baadhi ya wafanyabiashara kufanya biashara bila ya kujisajili TRA, baadhi ya wafanyabiashara biashara zao bado hawajakadiriwa, na baadhi yao hawatumii mashine za EFD ipasavyo.

Semeni ametoa wito kwa wafanyabiashara kuhakikisha wanasajili biashara zao, wanakadiriwa na kulipa kodi ya awamu kwa wakati ili kuiwezesha Serikali kukamilisha miradi ya maendeleo kwa wakati.








RUVUMA | Februari 28, 2026


Katibu Mkuu wa TRAMEPRO Atoa Wito wa Kugeuza Historia ya Vita vya Maji Maji kuwa Fursa za Maendeleo
Katibu Mkuu wa Shirika la Tiba Asili na Uhifadhi wa Mazingira (TRAMEPRO), Boniventura Mwalongo, leo Februari 28, 2026, amesema kuwa historia ya mashujaa wa Vita vya Maji Maji inapaswa kuenziwa kwa vitendo kwa kuigeuza kuwa chachu ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Mashujaa wa Vita vya Maji Maji yaliyofanyika Mkoa wa Ruvuma, Mwalongo alisema kuwa mashujaa hao walionesha ujasiri, umoja na uzalendo wa hali ya juu katika kupigania ardhi, heshima na utu wa Mwafrika.

“Damu ya mashujaa wa Vita vya Maji Maji ndiyo mbegu ya uhuru wetu. Ni wajibu wetu kuhakikisha historia yao haiishii kwenye kumbukumbu pekee, bali inakuwa sehemu ya maendeleo ya kizazi cha sasa na kijacho,” alisema Mwalongo.

Alisisitiza kuwa maadhimisho hayo yanapaswa kutumika kama jukwaa la kuhamasisha uwekezaji katika utalii wa kihistoria, tafiti za kisayansi pamoja na matumizi ya teknolojia katika kuhifadhi makumbusho na nyaraka muhimu za kihistoria.

“Tunaweza kugeuza maeneo ya kihistoria kuwa vivutio vya utalii, tukafungua ajira kwa vijana wetu na kuimarisha uchumi wa mkoa wetu. Hii ndiyo njia bora ya kuwaenzi mashujaa wetu,” aliongeza.

Aidha, aliwataka wadau mbalimbali kushirikiana katika kuhifadhi mazingira na kuendeleza tiba asili kama sehemu ya kulinda na kuenzi urithi wa taifa.

Maadhimisho ya Siku ya Mashujaa wa Vita vya Maji Maji Mkoa wa Ruvuma yameendelea kuwa kumbukumbu muhimu ya historia ya mapambano dhidi ya ukoloni, huku yakihamasisha kizazi cha sasa kujivunia utamaduni na urithi wao.

“Mashujaa wetu, tunawaenzi leo na milele,” alihitimisha Mwalongo.





 



Wananchi mbalimbali pamoja na baadhi ya viongozi wamepata fursa ya kutembelea onyesho maalum la Nduna Mkomanile lililofanyika katika Kituo cha Baraza la Wazee wa Mila na Desturi Mkoa wa Ruvuma.

Onyesho hilo limefanyika tarehe 27/02/2026, likiwakutanisha wadau mbalimbali waliotaka kujifunza na kutambua mchango wa wanawake katika historia ya ukombozi wa taifa.

Nduna Mkomanile anatambulika kama mwanamke shujaa, muhamasishaji na muwajibikaji katika jamii yake, aliyesimama imara wakati wa Vita vya Majimaji kupigania uhuru dhidi ya utawala wa kikoloni.

Lengo la onyesho hilo lilikuwa kuangazia mchango wa wanawake katika harakati za ukombozi dhidi ya wakoloni na kuonesha namna ambavyo mchango wao unaendelea kuonekana hata katika jamii ya sasa.

Onyesho hilo lilikuwa sehemu ya matukio ya Tamasha la Kumbukizi ya Vita vya Majimaji na Utalii wa Utamaduni, lililoratibiwa na Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Makumbusho ya Taifa kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma pamoja na Baraza la Wazee wa Mila na Desturi.

Kupitia onyesho hilo, wananchi wamepata nafasi ya kujifunza historia ya shujaa Nduna Mkomanile, namna alivyoshiriki katika Vita vya Majimaji na mapambano dhidi ya utawala wa kikoloni, pamoja na jukumu lake la kusambaza dawa wakati wa vita. Aidha, wamefahamu umaarufu wake, nafasi yake ya uongozi na ushauri, pamoja na mchango wake katika kuratibu mawasiliano wakati wa mapambano hayo.

Utafiti wa taarifa na maandalizi ya onyesho la Nduna Mkomanile yamewezeshwa na Women Fund Tanzania kupitia mtandao wa Kestoria, ikiwa ni muendelezo wa kampeni yao ya kuhakikisha historia za wanawake zinaibuliwa, zinaandikwa, zinatambuliwa na kusambazwa kwa kizazi cha sasa na kijacho.




















Meneja wa Ufungaji wa Mgodi wa Barrick Buzwagi, Mhandisi Zonnastraal Mumbi akitoa maelezo kwa Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Wallace Karia na ujumbe wake walipotembelea kituo cha michezo cha Buzwagi.

Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Wallace Karia na ujumbe wake wakitembelea maeneo mbalimbali ya kituo cha michezo cha Buzwagi.

Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Wallace Karia na ujumbe wake wakitembelea maeneo mbalimbali ya kituo cha michezo cha Buzwagi.

Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Wallace Karia na ujumbe wake wakitembelea maeneo mbalimbali ya kituo cha michezo cha Buzwagi.

Baadhi ya wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Taifa wa shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) wakiwa katika picha ya pamoja na Rais wa shirikisho hilo Wallace Karia na Meneja wa Ufungaji wa Mgodi wa Barrick Buzwagi, Mhandisi Zonnastraal Mumbi.


**

Mgodi wa Barrick Buzwagi ambao uko katika mchakato wa kufungwa kwa kushirikiana na Serikali umepongezwa kwa kuweka miundombinu ya kituo cha michezo ambacho kitasaidia kukuza mchezo wa soka na michezo mingineyo nchini.

Pongezi hizo zimetolewa na Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Wallace Karia, alipoongoza wajumbe wa Mkutano Mkuu wa taifa wa shirikisho hilo kutembelea eneo hilo ambapo amesema miundombinu iliyopo inaridhisha.

Amesema miundombinu hiyo kuanzia nyumba za malazi kwa wanamichezo, viwanja vya michezo, usalama, pamoja na mazingira yake kwa ujumla ipo katika hali nzuri na inakidhi mahitaji ya kuanzishwa kwa kituo hicho.

“Natoa shukrani kwa kampuni ya Barrick na Serikali kwa kukubali ombi la kuanzishwa kituo cha michezo katika eneo la mgodi uliofungwa, tunafurahi kuona kituo kiko katika hali nzuri na kina viwango vikubwa kwa ajili ya kuhudumia wanamichezo, hii ni fursa muhimu kwa maendeleo ya michezo yetu”, amesema.

Kwa upande wake Mjumbe wa Kamati Tendaji ya Taifa ya TFF, Azan Mufti, amesema kutengwa kwa eneo hilo kwa ajili ya wanamichezo kunadhihirisha ushirikiano mzuri uliopo kati ya sekta binafsi na wadau wa sekta ya michezo katika kufanikisha ajenda ya Serikali ya kukuza vipaji na kuendeleza michezo nchini.

Naye Meneja wa Ufungaji wa Mgodi wa Barrick Buzwagi, Mhandisi Zonnastraal Mumbi, amesema kutengwa kwa eneo la kujengwa kituo cha michezo katika eneo hilo la mgodi uliofungwa kumezingatia dhamira ya kampuni ya kusaidia jamii sambamba na kuunga mkono jitihada za serikali za kukuza vipaji na kuchochea maendeleo ya michezo nchini.
Mwaka 1976, Mtafiti wa masuala ya Akiolojia Dr. Mary Leakey aligundua nyayo za zamadamu eneo la Laetoli zilizohifadhika katika mwamba wa jivu la volcano iliyolipuka kwenye milima ya Ngorongoro zaidi ya miaka milion 3.6 iliyopita. Wataalamu wanaamini kuwa nyayo hizo ziliachwa na jamii ya watu wa kale waitwao Australopithecus Afarensis.

Nyayo za Zamadamu Laetoli Ngorongoro ni ushahidi usiopingika kuwa zamadamu (Hominin) wa umri wa miaka milioni 3.66 iliyopita walitembea wima kwa miguu miwili eneo la Laetoli Tanzania.

Kutembea wima kwa miguu miwili kunatutofautisha wanadamu na wanyama kama Sokwe na Nyani waliotokana na babu/bibi mmoja miaka takribani millioni 7 iliyopita.

Uwepo wa Nyayo na masalia ya binadamu, ndege na wanyama, urithi wa utamaduni, mambo kale, mimea, maji, matunda na kila kitu kinachomfanya binadamu kuishi ni kiashiria kuwa pengine bustani ya Eden ni Ngorongoro ni mahali ambapo tunda la mti wa katikati lililiwa.



NA. MWANDISHI WETU – Dar es Salaam

KATIBU Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Jim Yonazi ambaye pia ni mwenyekiti wa Kamati ya Usimamizi wa Mradi wa DART amesema Serikali imejipanga kikamilifu kuhakikisha inamaliza changamoto ya usafiri katika Jiji la Dar es Salaam, ili wananchi waweze kupata huduma bora, ya haraka na yenye uhakika.

Akizungumza mara baada ya Kamati hiyo kufanya ziara ya kukagua miundombinu ya usafirishaji jijini humo, Dkt. Yonazi amesema Serikali imewekeza kwa kiwango kikubwa katika kuboresha sekta ya usafiri wa umma.

Alisema katika ziara hiyo, kamati ilitembelea Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka Dar es Salaam (DART) pamoja na Kampuni ya Uendeshaji wa Mabasi Yaendayo Haraka (UDART) na kujionea maendeleo ya uwekezaji uliofanywa.

“Ni dhamira ya Serikali kuhakikisha usafiri wa Dar es Salaam unakuwa bora, wa kisasa na unaokidhi mahitaji ya wananchi. Tumejionea miundombinu iliyowekwa na jitihada zinazoendelea kuboresha huduma,” alisema.

Dkt. Yonazi alibainisha kuwa tayari kampuni zimeanza kuleta mabasi mapya, hatua itakayoliwezesha jiji hilo kuwa miongoni mwa majiji yenye usafiri wa kisasa barani Afrika. Aliongeza kuwa mabasi mengi yatatumia gesi asilia, huku Serikali ikiwa imejenga miundombinu ya vituo vya gesi ili kuhakikisha huduma hiyo inapatikana kwa urahisi.

Aidha, alisema Serikali imewekeza katika mifumo ya TEHAMA itakayomwezesha mwananchi kutumia kadi maalumu kulipia nauli bila kulazimika kupanga foleni, jambo litakaloongeza ufanisi na kupunguza usumbufu.

Katika hatua nyingine, aliwahakikishia wananchi kuwa mabasi yote yaliyoharibika yatafanyiwa ukarabati na kurejea barabarani ili kuimarisha upatikanaji wa huduma.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka Bw. Said Tunda alisema lengo kuu ni kurejesha furaha kwa wananchi wa Dar es Salaam kwa kuwapatia usafiri wa uhakika.

Pia aliwataka waendesha daladala kuendelea kutoa huduma huku Serikali ikiendelea kufanya mazungumzo nao ili kupata utaratibu bora wa ushirikiano, hususan kwa zile zilizopewa kibali cha kutumia barabara ya mwendokasi.

Hatua hizo zinaonesha dhamira ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Sita ya inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuboresha maisha ya wananchi kupitia miundombinu imara na huduma bora za kijamii.








Top News