Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amekagua Daraja la Mto Nyathorogo lililopo katika Kijiji cha Nyathorogo, Kata ya Nyathorogo, wilayani Rorya, mkoani Mara, ambalo limejengwa kwa lengo la kuboresha huduma za usafiri na usafirishaji kati ya wilaya za Rorya na Tarime.

Akiwa katika ziara yake ya kikazi mkoani Mara leo Jumatano, Julai 2, 2026, Waziri Mkuu alipokea taarifa ya utekelezaji wa mradi huo kutoka kwa Meneja wa TARURA Wilaya ya Rorya, Mhandisi Elifadhili Moses.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, mradi wa ujenzi wa daraja hilo umegharimu shilingi milioni 729.2 ulianza Agosti 1, 2025 na kukamilika Februari 28, 2026.

Mhandisi Moses alisema daraja hilo limejengwa kwa teknolojia ya mawe iliyowezesha kupunguza gharama za ujenzi kwa zaidi ya asilimia 50 ikilinganishwa na usanifu wa awali, na kwamba Serikali imetenga fedha katika mwaka wa fedha 2026/2027 kwa ajili ya ujenzi wa kingo za kulinda daraja dhidi ya athari za maji.

Naye Mbunge wa Jimbo la Rorya,  Jafari Chege alisema daraja hilo limeondoa adha ya muda mrefu iliyokuwa ikiwakabili wananchi wa Rorya na Tarime, ambapo awali walilazimika kuvuka Mto Nyathorogo katika mazingira hatarishi yaliyosababisha ajali na kupoteza maisha.

Aidha, alisema ujenzi wa daraja hilo umeboresha mawasiliano kati ya wilaya hizo mbili na kurahisisha upatikanaji wa huduma za kijamii na shughuli za kiuchumi kwa wananchi wa maeneo hayo.













Na Mwandishi Wetu- Dodoma

Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania (TFNC) Bi. Debora Charwe amesema, Serikali ipo katika mchakato wa kuandaa Mpango wa Muda Mrefu wa Lishe wa Taifa (NN-LTP) ili kuongeza jitihada za sekta mtambuka katika kuboresha utekelezaji wa lishe kwa kipindi cha miaka 25 ijayo

Bi. Debora ameyasema hayo leo tarehe 30 Juni, 2026 wakati akifungua Warsha ya mafunzo kuhusu kuandaa mpango wa muda mrefu wa lishe wa Taifa (National Nutrition Long Term Plan 2026-2050) ambayo inafanyika jijini Dodoma kwa siku tatu kuanzia Juni 30 hadi Julai 02, 2026



Amesema, mafunzo hayo yanatolewa kwa Wataalam kutoka ngazi ya Wizara mbalimbali kwa lengo la kuwajengea uwezo kuhusu uandaaji wa mipango ya muda mrefu wa lishe inayojumuisha sekta mtambuka pamoja na kubadilishana uzoefu kusaidia katika usanifu, muundo na taratibu za utekelezaji wa Mpango wa muda mrefu wa Lishe wa Taifa.


















Vilevile Bi. Debora amefafanua kuwa, mpango huo unaandaliwa chini ya usimamaizi wa Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania (TFNC) na wadau wengine wa maendeleo kwa kuzingatia haja ya kuifanya lishe kuwa moja ya kichocheo na kipimo katika kufikiwa kwa malengo ya Dira ya Maendeleo ya Tanzania kufikia 2050.

Aidha, warsha hiyo imehusisha Afisa viungo wa lishe kutoka Wizara mbalimbali zikiwemo Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana, Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano) pamoja na Wizara ya Kilimo, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Viwanda, Wizara ya Maji na Wizara ya Mambo na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
Maafisa Biashara kutoka Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma leo tarehe 1 Julai, 2026 wametembelea Banda la Halmashauri ya Jiji la Dodoma katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba) yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam.

Wakiwa katika banda hilo, maafisa hao walipata maelezo kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa na Halmashauri ya Jiji la Dodoma, ikiwemo ushauri na miongozo kwa wananchi na wawekezaji kuhusu upatikanaji wa maeneo ya uwekezaji na huduma za ardhi, fursa za biashara katika sekta za kimkakati zinazokuwa kwa kasi pamoja na taratibu za uwekezaji ndani ya jiji

Akizungumza baada ya kutembelea banda hilo, Mkuu wa Divisheni ya Biashara, Viwanda na Uwekezaji kutoka Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro, Lusajo Mwasongwe alisema kuwa wamejifunza mambo mbalimbali yanayoweza kuwasaidia kuboresha utoaji wa huduma katika mamlaka zao. “Tumepata uzoefu mzuri katika banda hili kuhusu namna Jiji la Dodoma linavyotangaza fursa za uwekezaji na kutoa huduma kwa wananchi” alisema Mwasongwe.

Kwa upande wake, Afisa Biashara wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Ruth Kingu alisema kuwa maonesho hayo yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kuitangaza halmashauri na kuvutia wawekezaji pamoja na wadau mbalimbali. “Tunawakaribisha wananchi, wafanyabiashara na wawekezaji kutembelea banda letu ili kupata huduma na kufahamu fursa mbalimbali zilizopo ndani ya Jiji la Dodoma" alisema Kingu.

Halmashauri ya Jiji la Dodoma inaendelea kushiriki katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara kwa lengo la kutangaza huduma zake, kuonesha fursa za uwekezaji na kuimarisha ushirikiano na wadau mbalimbali wa maendeleo.







Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga (Mb) , amesema Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) yameonyesha mafanikio makubwa ya sekta ya viwanda na biashara pamoja na fursa zinazotolewa na Serikali kwa vijana na wanawake.

Waziri Kapinga amesema hayo akiwa ameambatana na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Balozi Waziri Salum, alipotembelea maonesho hayo julai 01, 2026 yanayoshirikisha waoneshaji 3,722 kutoka nchi 23 ambayo yatafunguliwa rasmi Julai 3 na Rais wa Msumbiji, Mhe. Daniel Francisco Chapo, akiwa ameambatana na Rais wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Aidha, amewataka Watanzania kutembelea maonesho hayo ili kujifunza kuhusu biashara, viwanda na fursa za kuongeza thamani ya mazao.

Amesema bidhaa nyingi zinazozalishwa na wanawake na vijana zinaonesha matokeo ya uwekezaji wa Serikali kupitia mikopo na programu za uwezeshaji.

Na Munir Shemweta, Dar es Salaam

Serikali imetangaza kuanza kutoa vibali vya ujenzi na kufanya majadiliano na wamiliki wa ardhi na nyumba ambao wapo tayari kushiriki kwenye Mpango wa Uendelezaji Upya eneo la Sinza, huku ikisisitiza kuwa mchakato uliopita umefutwa ili kutoa nafasi ya kuanza upya kwa misingi ya uwazi, ushirikishwaji na kujenga maridhiano.

Kauli hiyo ilitolewa Julai 1, 2026 jijini Dar es Salaam na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt. Leonard Akwilapo, alipokutana na wamiliki wa ardhi na nyumba wa Sinza kwa lengo la kuwafafanulia hatua za utekelezaji wa mpango huo na kusikiliza maoni yao.

Dkt. Akwilapo alisema Serikali imeamua kufungua ukurasa mpya baada ya kubaini kuwa mchakato uliopita uliacha malalamiko kutoka kwa baadhi ya wananchi, hivyo vikao vyote vya awali vimefutwa na sasa mazungumzo yanaanza upya kwa ushirikiano na wananchi.

Alieleza kuwa ukuaji wa miji ni jambo lisiloepukika kutokana na ongezeko la watu na mahitaji ya makazi, hivyo Serikali ina wajibu wa kupanga matumizi ya ardhi kwa kuzingatia mahitaji ya sasa na ya baadaye.

Waziri huyo alisema Sinza ya sasa imebadilika kwa kiwango kikubwa ikilinganishwa na ilivyokuwa miaka ya nyuma, jambo ambalo linahitaji mpango mpya wa maendeleo utakaoendana na hadhi yake kama eneo muhimu la makazi na biashara ndani ya Jiji la Dar es Salaam.

"Kama mwananchi anaona mpango huu haufai, hiyo ni haki yake, lakini ipo siku ataona umuhimu wake. Tusiporatibu maendeleo ya miji, tutakuwa na maeneo yasiyo na mpangilio na yenye miundombinu isiyokidhi mahitaji ya wananchi," alisema.

Dkt. Akwilapo alibainisha kuwa uendelezaji upya wa maeneo ya makazi si jambo geni nchini, kwani maeneo kama Posta, Kariakoo, Upanga, Oysterbay na Masaki yamepitia hatua kama hizo na yameendelea kuwa na thamani kubwa zaidi kutokana na upangaji mzuri wa matumizi ya ardhi.

Waziri huyo aliwataka wananchi kuwa makini na watu wasio waaminifu wanaoweza kutumia mchakato huo kuwahadaa au kuwasambazia taarifa zisizo sahihi kwa manufaa binafsi.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, alisema mafanikio ya mpango huo yatategemea kiwango cha ushirikishwaji wa wananchi na kuzingatia maoni yao.

Alipendekeza muda wa ukusanyaji wa maoni uongezwe kwa miezi mitatu ili wananchi wengi zaidi wapate nafasi ya kuelewa mpango huo na kutoa maoni yao kabla ya hatua za utekelezaji kuanza.

"Wananchi wasikilizwe, maoni yao yazingatiwe na rasimu iboreshwe ili iakisi matakwa yao. Serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan haiwezi kupora haki za wananchi bali itafuata sheria, kanuni na taratibu zote zinazotambuliwa," alisema Profesa Mkumbo.

Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhandisi Anthony Sanga aliwataka wamiliki wa ardhi na nyumba wa Sinza kuwa watulivu na kutochukua maamuzi ya haraka ya kuuza maeneo yao kutokana na taarifa zisizo rasmi.

Alisema thamani ya ardhi katika eneo la Sinza imeongezeka maradufu hivyo wananchi wanapaswa kutambua fursa iliyopo badala ya kufanya maamuzi yatakayowagharimu baadaye.

Akizungumza kwa niaba ya Kamati ya Wamiliki wa Ardhi na Nyumba wa Sinza, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Bw. Asibwene Lumuli, alisema ushirikiano kati ya Serikali na wananchi ndio utakaohakikisha mpango huo unatekelezwa kwa mafanikio na kwa manufaa ya pande zote.Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Leonard Akwilapo akizungumza na wamiliki wa ardhi na Nyumba Sinza wakati wa Kikao kujadili uendelezaji upya eneo la Sinza Dar es Salaam tarehe 1 Julai 2026.Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Leonard Akwilapo akizungumza na baadhi ya wamiliki wa ardhi na Nyumba Sinza mara baada ya Kikao kujadili uendelezaji upya eneo la Sinza Dar es Salaam tarehe 1 Julai 2026.Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhandisi Anthony Sanga akizungumza katika kikao kati ya waziri wa Ardhi na wamiliki wa ardhi na Nyumba Sinza wakati wa Kikao kujadili uendelezaji upya eneo la Sinza Dar es Salaam tarehe 1 Julai 2026.Meya wa Manispaa ya Ubungo Mstahiki Lawrence Mlaki akizungumza wakati wa kikao kati ya waziri wa Ardhi na wamiliki wa ardhi na Nyumba Sinza wakati wa Kikao kujadili uendelezaji upya eneo la Sinza Dar es Salaam tarehe 1 Julai 2026.Mwenyekiti wa Kamati ya wamiliki wa ardhi na Nyumba Sinza Bw. Asibwene Lumuli akizungumza katika kati ya waziri wa Ardhi na wamiliki wa ardhi na Nyumba Sinza wakati wa Kikao kujadili uendelezaji upya eneo la Sinza Dar es Salaam tarehe 1 Julai 2026.Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Leonard Akwilapo akisalimiana na Mkuu wa wilaya ya Ubungo Bw, Albert Msando wakati wa Kikao kujadili uendelezaji upya eneo la Sinza Dar es Salaam tarehe 1 Julai 2026.Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Leonard Akwilapo akiwa katika picha ya pamoja na kamati ya wamiliki wa ardhi na Nyumba Sinza mara baada ya Kikao kujadili uendelezaji upya eneo la Sinza Dar es Salaam tarehe 1 Julai 2026.Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Leonard Akwilapo akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wamiliki wa ardhi na Nyumba Sinza mara baada ya Kikao kujadili uendelezaji upya eneo la Sinza Dar es Salaam tarehe 1 Julai 2026.Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo akizungumza wakati wa Kikao kujadili uendelezaji upya eneo la Sinza Dar es Salaam tarehe 1 Julai 2026. (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)

 

Kufuatia mwaliko wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Daniel Francisco Chapo Rais wa Jamhuri ya Msumbiji, anatarajiwa kuanza ziara ya kikazi ya siku tatu nchini kuanzia tarehe 02 hadi 04 Julai, 2026.

 Wakati wa ziara hiyo, Mheshimiwa Rais Chapo anatarajiwa kufanya mazungumzo rasmi na mwenyeji wake, Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

 Mazungumzo hayo yatajikita katika kuimarisha ushirikiano wa pande mbili katika nyanja mbalimbali zikiwemo biashara, uwekezaji, uchukuzi, nishati pamoja na kuangazia maeneo mapya ya ushirikiano yenye maslahi ya pamoja kwa wananchi wa nchi hizi mbili. 

Mnamo tarehe 03 Julai 2026, Mheshimiwa Rais Chapo anatarajiwa kufungua rasmi Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (DITF), maarufu kama Sabasaba, yatakayowakutanisha wafanyabiashara, wawekezaji na wadau mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi kwa lengo la kukuza biashara, uwekezaji na ushirikiano wa kiuchumi. 

Aidha, Mheshimiwa Rais Chapo atamtembelea Mama Maria Nyerere, Mjane wa Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kwa lengo la kutoa heshima na kutambua mchango wa viongozi waasisi katika kuimarisha uhusiano wa kindugu kati ya Tanzania na Msumbiji, hususan wakati wa harakati za ukombozi wa Bara la Afrika.

 Ziara ya Mheshimiwa Rais Chapo ni kielelezo cha uhusiano imara wa kihistoria na ushirikiano wa karibu kati ya Tanzania na Msumbiji, na inatarajiwa kuendelea kufungua fursa mpya za ushirikiano katika nyanja mbalimbali za maendeleo.

 Itakumbukwa kuwa, ziara hii ni ya tatu kwa Mheshimiwa Rais Chapo nchini Tanzania tangu alipoingia madarakani mwaka 2024, jambo linaloakisi dhamira ya viongozi wa nchi hizi mbili ya kuendelea kuimarisha mahusiano ya kirafiki na ushirikiano wa karibu, yaliyojengwa juu ya historia ya ujirani mwema na mshikamano wa muda mrefu.


NA DENIS MLOWE, IRINGA


MBUNGE wa Jimbo la Isimani, Emanuela Mtatifikolo Kaganda, ametoa msaada wa mabati kwa waendesha bodaboda wa kijiji cha Itunundu kilichoko kata ya Itunundu jimbo la Ismani kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa kijiwe chao cha kusubiri abiria, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono jitihada zao za kuboresha mazingira ya kazi.

Akizungumza kabla ya kukabidhi msaada huo, Mtatifikolo alisema kuwa bodaboda ni kundi muhimu katika kuchochea uchumi na kutoa huduma za usafiri kwa wananchi, hivyo linastahili kupewa ushirikiano na mazingira bora ya kufanyia kazi.

Alieleza kuwa ujenzi wa kijiwe hicho utawasaidia waendesha bodaboda kupata sehemu salama na yenye staha ya kusubiri wateja, sambamba na kuimarisha mpangilio wa shughuli zao.

Mbunge huyo aliwataka wanufaika kuhakikisha wanatumia mabati hayo kwa lengo lililokusudiwa na kukamilisha ujenzi wa kijiwe hicho kwa wakati, huku akisisitiza umuhimu wa kutunza miundombinu hiyo mara baada ya kukamilika.

Kwa upande wao, waendesha bodaboda walimshukuru Mbunge huyo kwa msaada alioutoa, wakisema utachangia kwa kiasi kikubwa kukamilisha ujenzi wa kijiwe hicho na kuboresha mazingira yao ya kazi pamoja na huduma wanazozitoa kwa wananchi.

Walisema kuwa kutokana na joto kali la tarafa ya Pawaga ambapo inapatikana kijiji cha Itunundu msaada huo utasaidia kuepukana na hali hiyo kitu ambacho mbunge amejitoa kwa lengo la kusaidia vijana.





Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali imeelekeza halmashauri zote nchini kutenga asilimia tano ya mapato yao ya ndani kwa ajili ya ujenzi na uboreshaji wa miundombinu ya biashara ili kuwawezesha wananchi, hususan vijana na wanawake, kufanya shughuli za kiuchumi katika mazingira bora na yenye tija.

Akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika Uwanja wa Ingwe Sekondari, Jimbo la Tarime Vijijini, wilayani Tarime, mkoani Mara, leo Jumatano, Julai 1, 2026, Waziri Mkuu alisema hatua hiyo inalenga kuondoa changamoto za maeneo ya biashara na kuongeza fursa za uzalishaji na ajira.

"Tumeenda kuweka asilimia tano kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya maeneo ya biashara. Na kwenye hiyo asilimia tano, nimewaelekeza wenzetu wa TAMISEMI kwamba kama kuna eneo vijana wanalitaka kwa ajili ya kufanyia biashara, hata kama hilo eneo lina wamiliki, tumieni asilimia tano kulinunua. Msiwapeleke vijana kufanyia biashara maeneo ya mbali ambayo hayaendani na biashara wanazozifanya."

Aidha, Waziri Mkuu alisema Serikali imepitisha utaratibu wa kuwapa wafanyabiashara wanaoanzisha biashara mpya kipindi cha mwaka mmoja kabla ya kuanza kulipa kodi, ili kuwapa nafasi ya kuimarisha biashara zao.

"Wale vijana na kina mama wanaoanzisha biashara mpya hawataanza kudaiwa kodi mara wanapoanzisha biashara. Sasa watakuwa na likizo ya mwaka mzima ili wajipange katika kuimarisha biashara zao."

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu alisema Serikali itawasilisha bungeni marekebisho ya sheria inayohusu kutaifisha mifugo kwa lengo la kuondoa adhabu ambazo zimekuwa zikiwaathiri wafugaji bila kuathiri juhudi za uhifadhi.

"Bunge lijalo la mwezi wa nane tunaenda kufuta sheria inayotaifisha mifugo ya Watanzania. Tumetathmini tukagundua kwamba sheria hiyo inawatia umaskini Watanzania. Tumegundua katika baadhi ya maeneo adhabu imekuwa kubwa kuliko kosa lililotendwa."

Pia, Waziri Mkuu alisema Serikali imeelekeza kusitishwa kwa utaratibu wa kukamata vitendea kazi vya wananchi kwa madai ya faini, akisema hatua hiyo imekuwa ikikwamisha shughuli za uzalishaji na kujiongezea kipato.

"Kama mtu anadaiwa faini, mwacheni kitendea kazi chake, aendelee kufanya kazi ili awalipe faini. Tuache utekelezaji wa sheria wa kishamba shamba."

Sambamba na hayo, Waziri Mkuu alisisitiza kuwa Serikali haitavumilia ubadhirifu na matumizi mabaya ya madaraka katika utumishi wa umma.

"Mtu akiiba, mtumishi wa umma akiiba, msimhamishe. Mfukuzeni kazi. Hatuna uhaba wa watu wa kufanya kazi."

Akihitimisha, Waziri Mkuu aliwataka wananchi kuendelea kulinda amani, umoja na usalama wa nchi, akisisitiza kuwa maendeleo ya taifa na ustawi wa wananchi unategemea kuwepo kwa mazingira ya amani, utulivu na mshikamano.







Top News