Na Mwandishi Wetu Michuzi Tv

VIJANA nchini wameungana kuadhimisha Siku ya Kumbukizi ya kuzaliwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, wakisema kuwa ni kiongozi mlezi wa vijana na chachu ya maendeleo ya taifa kwa vitendo.

Akizungumza katika hafla hiyo iliyofanyika leo Januari 27,2026 Mratibu wa Taasisi ya Together for Samia ambaye pia ni Muandaaji wa shaghuli hiyo, Gulatone Masiga amesema tukio hilo limeandaliwa na vijana kwa hiari yao kama ishara ya upendo, heshima na kuthamini mchango wa Rais Samia katika kuwekeza maendeleo ya vijana na taifa kwa ujumla.

“Tuliona tufanye shughuli itakayotuleta pamoja, ikiwa ni nafasi ya sisi vijana kuonyesha upendo wetu kwa Rais wetu mama na mlezi wa vijana, ambaye ametujali na kuwekeza kwa vitendo katika maendeleo yetu,” amesema Masiga

Amesema vijana wengi waliokuwepo ni wa kizazi kipya ambacho kimenufaika kwa kiasi kikubwa na uongozi wa Rais Samia katika kipindi cha takribani miaka mitano, hususan kupitia ujenzi wa vyuo vya ufundi na ujuzi katika zaidi ya wilaya 62 nchini, hatua iliyowezesha vijana kupata maarifa na ujuzi wa kujiajiri.

Masiga ameongeza kuwa mageuzi katika sekta ya elimu kupitia mtaala unaozingatia maarifa (knowledge-based curriculum) umehakikisha wahitimu wa elimu ya msingi na sekondari wanapata vyeti vya elimu ya kawaida sambamba na vyeti vya ufundi (VETA), hali inayowawezesha kuingia kwenye soko la ajira au kujiajiri.

Katika sekta ya nishati, amesema uwekezaji mkubwa wa serikali, ikiwemo mradi wa zaidi ya shilingi trilioni moja wa kupeleka umeme katika vitongoji 99 nchi nzima, umefungua fursa nyingi za kiuchumi kwa vijana, wakiwemo mafundi seremala, welders, wajasiriamali wa saluni, car wash na shughuli nyingine za uzalishaji.

“Tunaona wazi kwamba uwekezaji huu ni fursa ya moja kwa moja kwa vijana,” amesema.

Ameeleza pia kuwa miradi mikubwa ya miundombinu ikiwemo reli ya kisasa (SGR) inayounganisha mikoa mbalimbali nchini itakapokamilika, vijana watakuwa miongoni mwa wanufaika wakuu kupitia ajira na shughuli za kiuchumi.

Kwa upande wa sekta ya afya, vijana hao wamepongeza ujenzi wa vituo vya afya hadi ngazi ya kata pamoja na kuanza kwa mpango wa bima ya afya kwa wote, ambapo kaya zitalipia kiasi cha shilingi 150,000 kwa familia yenye watu sita, huku makundi maalum yakigharamiwa na serikali.

Mmoja wa vijana walioshiriki hafla hiyo, Dorcas Mshiu ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa muanzilishi wa Vijana Innovation, amesema Rais Samia amefungua fursa nyingi za kiuchumi kwa vijana, ikiwemo urahisishaji wa usajili wa biashara na kuvutia wawekezaji nchini.

“Mama yetu hajatuacha.

Amesema kuwa Rais Samia ametengeneza mazingira rafiki kwa vijana kujiajiri, ikiwemo mikopo ya asilimia mbili na nne kupitia halmashauri. Hii ni serikali inayowaamini vijana,” amesema Doras.

Vijana hao wamesema sababu ya kuadhimisha siku hiyo ni kutambua uongozi wa Rais Samia unaojengwa juu ya misingi ya maridhiano, amani na umoja wa kitaifa, wakiahidi kuendelea kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo ya taifa.





Mbunge wa Jimbo la Kibamba, Mkuu wa Wilaya ya Ubungo (DC) pamoja na watendaji wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) wamekutana katika kikao kazi kilicholenga kutafuta suluhisho la changamoto ya upatikanaji wa huduma ya maji katika jimbo la Kibamba.

Akizungumza katika kikao hicho, Mbunge wa Kibamba, Mheshimiwa Angella Kairuki, amesema changamoto ya maji imekuwa kero kubwa kwa wananchi wa Jimbo hilo, hali inayohitaji hatua za haraka na za kudumu ili kuboresha upatikanaji wa huduma hiyo.

Amesema kuna umuhimu wa kuwa na chanzo zaidi ya kimoja katika Jimbo hili, hivyo kazi ya kutambua na kupata maeneo ya uchimbaji wa visima vya maji inabidi ifanyike ikiwa ni mkakati wa kuongeza vyanzo vya maji na kupunguza utegemezi wa miundombinu ya sasa.

“Kipaumbele chetu ni kutambua maeneo sahihi ya kuchimba visima vya maji ili kuongeza vyanzo vya maji na kupunguza adha kwa wananchi, kwa sababu tutakapokuwa na vyanzo vingine vya huduma ni vigumu sana wananchi kulalamika kwa muda mrefu juu ya ukosefu wa maji,” amesema Mheshimiwa Kairuki.

Mheshimiwa Mbunge amesema utekelezaji wa mpango wa uchimbaji wa visima vya maji, sambamba na maboresho ya mtandao wa usambazaji wa maji, utawezesha wananchi kupata huduma ya maji kwa uhakika, hasa katika maeneo yenye changamoto kubwa.

“Nawaomba watendaji wa DAWASA kuhakikisha maeneo ya uchimbaji wa visima yanapatikana kwa haraka ili utekelezaji wake uanze na kuondoa adha hii kwa wananchi,” amesema Mheshimiwa Kairuki ambaye pia ni Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Albert Msando amesema Serikali itaendelea kushirikiana kwa karibu na DAWASA ili kuhakikisha changamoto ya huduma ya maji katika Jimbo la Kibamba inapatiwa ufumbuzi wa kudumu na inaunga mkono juhudi zote za kitaalamu zitakazolenga kuboresha upatikanaji wa maji kwa wananchi.

Kwa niaba ya watendaji wa DAWASA katika jimbo la Kibamba, Ndugu Tumaini Mhondwa amesema tayari wanafanya tathmini ya kitaalamu ya maeneo mbalimbali kwa lengo la kubaini vyanzo vipya vya maji, ikiwemo uchimbaji wa visima, pamoja na kuboresha miundombinu ya usambazaji wa maji ili kuimarisha huduma ya maji katika jimbo hilo.



Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa( Mb.) amekutana na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TABD) na kufanya mazungumzo na yanayolenga kuendeleza ushirikiano kati ya wizara na benki hiyo na kuitaka kuendeleza miradi ya sekta za mifugo na uvuvi.

Mazungumzo hayo yamefanyika leo 27 Januari 2026 katika ofisi ndogo ya Wizara hiyo iliyopo Kambarage Tower Jijini Dodoma, ambapo Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya TADB alifika kujitambulisha kwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi na kuimarisha ushirikiano kati ya Wizara hiyo na Benki ya TADB katika kuendeleza sekta za Mifugo na Uvuvi.

Katika Mazungumzo hayo Mhe. Balozi Dkt. Bashiru ameipongeza Benki ya TADB kwa jinsi inavyoshirikiana na wizara na kuiagiza kupanua wigo wa kuwasaidia wafugaji wadogo kupata mikopo nafuu ili waweze kuendeleza miradi yao, pamoja na kuongeza ushiriki wa Taasisi za kifedha kupitia TADB katika kutoa mikopo kwenye Sekta ya Mifugo na Uvuvi.

Kwa upande wa Mkurugenzi Mtendaji wa TADB Bw. Frank Nyabundege amempongeza Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa kwa kuteuliwa kuwa Mbunge na Waziri wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi na kuahidi kuongeza kasi ya utoaji mikopo kwenye Sekta ya Mifugo na Uvuvi hasa kwenye miradi inayowalenga vijana na wanawake.

Aidha, Bw. Nyabundege aliwasilisha taarifa fupi kuhusu ushiriki wa TADB katika Maendeleo ya Sekta ya Mifugo na Uvuvi nchini ambapo kupitia TADB kama Benki ya Kisera inashirikiana na Wizara ya Mifugo na Uvuvi katika kutekeleza miradi mbalimbali inayolenga kuleta maendeleo katika Sekta ya Mifugo na Uvuvi ikiwemo Benki kutoa mikopo ya mradi wa boti, ufugaji samaki kwa njia ya vizimba na mikopo ya vijana kupitia Programu ya BBT mifugo.

Kupitia mikopo ya miradi ya boti na vizimba TADB ilipokea kiasi cha Shilingi Bilioni 34.9 kwa ajili ya kutekeleza mradi ambapo hadi sasa kiasi cha Shilingi Bilioni 29.83 kimetolewa kwa wanufaika 5,932 katika mikoa 16 hapa nchini.

Aidha, TADB kwa kushirikiana na Wizara ya Mifugo na Uvuvi imefanikiwa kutoa jumla ya boti 219 na vizimba 536 kwa wanufaika wa miradi. Aidha, kwa kupitia mradi wa vijana wa BBT Mifugo, kiasi cha Shilingi Milioni 847.3 kimetolewa kwa wanufaika 106 kwa miradi ya mikopo isiyo na riba.

Bw. Nyabundege aliongezea kuwa TADB imewasilisha ushiriki wake katika kutoa mikopo katika Sekta ndogo ya Maziwa nchini kupitia Mradi wake wa TI3P ambapo kiasi cha Shilingi 40bn kimetolewa kwa wafugaji na wasindikaji wa maziwa nchini.

 Aidha, kupitia mradi wa TI3P TADB imefanikiwa kurekebisha na kujenga vituo 23 vya kukusanya maziwa vyenye thamani ya Shilingi 1.1bn kwa kushirikiana wafugaji,Wizara, Halmashauri na wasindikaji wa maziwa.

 

Miti imekuwa muhimili muhimu katika ukuaji wa sekta ya viwanda na biashara kwani kupitia miti, viwanda hupata malighafi, biashara hukua, na uchumi huimarika.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga (Mb.), Januari 27, 2026, akiwa ameambatana na Naibu Waziri,Mhe. Dennis Londo pamoja na Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Bw. Needpeace Wambuya kushiriki zoezi la kupanda miti katika Ofisi za Wizara hiyo zilizopo Mji wa Serikali, Mtumba, jijini Dodoma. 

Zoezi hilo ni sehemu ya kusherehekea kumbukizi ya siku ya kuzaliwa ya Mwanamazingira namba moja hapa nchini, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye aliazimisha siku yake 27 Januari, 1960 kwa kupanda mti wa Muembe (Mangifera indica) katika eneo la Bungi Kilimo, Mkoa wa Kusini Unguja tarehe 27 Januari, 2026.

Aidha, Waziri Kapinga wakati akiongea na Watumishi wa Wizara hiyo baada ya kupanda mti, Altria rai kwa watumishi wa wizara kuhakikisha kila mmoja anashiriki kikamilifu katika upandaji miti ili kusaidia uhifadhi wa mazingira na kuibadili Dodoma kuwa ya kijani.

Uhifadhi na utunzaji wa miti unachangia kwa kiasi kikubwa katika sekta ndogo ya uchakataji wa mazao ya misitu, hususan utengenezaji wa mbao na samani, ambayo ni moja ya nyanja muhimu katika kukuza maendeleo endelevu ya sekta ya viwanda na biashara nchini

Farida Mangube, Morogoro 

Taasisi ya Utafiti wa Misitu Tanzania (TAFORI) leo Januari 27, 2026 imeshiriki Kampeni ya Kitaifa ya Upandaji Miti #27Yakijani kwa kupanda miti ya asili aina ya Mkongo (Afzelia quanzensis), kama sehemu ya kuunga mkono juhudi za Serikali katika uhifadhi wa mazingira na kuadhimisha siku ya kuzaliwa ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Zoezi hilo liliongozwa na Mkurugenzi Mkuu wa TAFORI, Dkt. Revocatus Mushumbusi, kwa kushirikiana na Watumishi wa Taasisi hiyo kutoka Makao Makuu na Vituo vya Utafiti, na kufanyika katika moja ya maeneo ya shamba la miti la Taasisi. 

Akizungumza na Waandishi wa habari, Dkt. Mushumbusi alisema upandaji wa miti ya Mkongo unalenga kurejesha miti ya asili yenye thamani kubwa na iliyo hatarini kutoweka, sambamba na kuimarisha uhifadhi wake.

Aliongeza kuwa ushiriki wa TAFORI katika kampeni hiyo ni sehemu ya kutimiza wajibu wa kitaasisi wa kufanya utafiti, kuratibu na kusambaza matokeo ya utafiti wa misitu na ufugaji nyuki, kwa lengo kuu la kuendeleza uhifadhi miti ya asili na mingineyo, ikiwa ni pamoja na kuendelea kuonesha mfano wa namna sahihi ya upandaji wa miti katika maeneo husika.

Zoezi la 27Yakijani linaongozwa na kaulimbiu “Uzalendo ni Kutunza Mazingira, Shiriki Kupanda Miti”, kaulimbiu inayoakisi dhamira ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuendeleza ajenda ya Taifa ya uhifadhi wa mazingira, ikiwemo upandaji miti, ulinzi wa vyanzo vya maji, kuimarisha uoto wa asili na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Kadhalika, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameadhimisha siku yake ya kuzaliwa kwa kupanda mti wa muembe (Mangifera indica) katika eneo la Bungi Kilimo, Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar, kama Kiongozi na mdau wa mfano katika kulinda na kutunza mazingira.








📍Atimiza ndoto yake ya siku nyingi ya kuitembelea Tanzania
WAZIRI  wa Maliasili na Utalii Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) amempokea shabiki mashuhuri wa klabu ya Manchester City ya Uingereza Braydon Bent ambaye ametimiza ndoto yake ya siku nyingi ya kuitembelea Tanzania na kujionea vivutio mbalimbali ikiwemo Serengeti na Mlima Kilimanjaro.

Ni kama safari iliyochukua karne hivi ya kutoka tu Etihad Stdium hadi Serengeti! Shabiki huyo mtopezi wa Manchester City anasifika kwa kurekodi video akiongea Kiswahili na alipata kuahidiwa kuja Tanzania tangu mwaka 2020.

Leo, hatimaye, Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt. Hassan Abbasi wametimiza ndoto ya shabiki huyo ambaye amepata pia kuwahoji mastaa kama Neymar, Aguero, Kocha Pep Guadiola na sasa akiwa mtangazaji wa mechi za Man City na pia akiwa na vipindi Sky News.

“Ilikuwa ndoto yangu kubwa kufika nchi hii nzuri. Kwa mapokezi haya naona kabisa tayari safari yangu imeanza vyema kabisa,” alisema Braydon akiwa ameambatana na Bw. Mark Bent, baba yake mzazi.
Karibu kwenye nchi bora kwa Utalii wa safari duniani.



Afisa Uhusiano na Huduma kwa Wateja TANESCO Mkoa wa Ruvuma Alan Njiro, amesema kuwa umeme ni nishati muhimu lakini ni hatari endapo hautatumika kwa usahihi, kwani unaweza kusababisha madhara makubwa kwa jamii.

Njiro ameyasema hayo Januari 27 alipotembelea shule ya msingi Mwenge na Shule ya sekondari Nasuri iliyopo Wilayani Namtumbo mkoani Ruvuma wakati wa mwendelezo wa ziara yake ya utoaji wa elimu ya matumizi salama ya umeme kwa wananchi na wanafunzi wa shule za msingi na sekondari,  kuhusu faida na athari za umeme.

Kwa mujibu wa Njiro, elimu hiyo inalenga kuwajengea wanafunzi uelewa mapema ili waweze kujilinda dhidi ya hatari za umeme na pia kuifikisha elimu hiyo kwa familia na jamii zao.

Ameeleza kuwa transfoma hutumika kupoza umeme kabla ya kusambazwa majumbani, hivyo ni hatari kwa mtu yeyote kuichezea au kukaribia miundombinu hiyo.

Njiro amewataka watoto kutoa taarifa kwa wazazi au walezi wao pindi wanapoona mtu akichezea transfoma au nyaya za umeme, ili hatua za haraka zichukuliwe, ameongeza kuwa ushirikiano kati ya TANESCO na jamii ni muhimu katika kuzuia ajali zinazoweza kujitokeza.

TANESCO Ruvuma imeendelea kutoa elimu kwa wananchi kama sehemu ya mkakati wa kupunguza madhara yatokanayo na umeme, na kulinda miundombinu kwa kuzingatia  majukumu yake muhimu ya kuzalisha, kusafirisha, kusambaza na kuuza umeme nchini.






 

Na. Janeth Raphael MichuziTv - Dodoma 

‎Naibu waziri wa Viwanda na Biashara Dennis Londo, amesema kuwa ujio mpya wa stakabadhi za ghala unawakumbusha wakulima changamoto walizopitia kupitia vyama vyao vya ushirika. Aidha, amebainisha kuwa kazi kubwa iliyopo sasa ni kuimarisha imani ya wananchi kwa serikali na taasisi zake, ikiwemo mfumo huu wa stakabadhi za ghala.

Londo ‎ameyazungumza  hayo wakati WRRB Uzinduzi wa Mfumo na kuazimisha Miaka 20 ya Kuimarisha Biashara ya Kilimo Tanzania Kupitia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala 27, 2026, Jijini Dodoma.

‎Amesema, "Ujio mpya wa stakabadhi ghalani na yenyewe pia inawakumbusha changamoto wakulima hawa kule walikotokea kupitia vyama vyao vya ushirika. Kazi kubwa ambayo nayo sasa hivi ni imani ya wananchi kwa serikali. Imani ya wakulima kwa taasisi za Serikali na mifumo ya Serikali ikiwemo hii ya stakabadhi za ghala." amesema waziri Londo

‎AmeelezaAmeeleza kuwa, "Wakulima wanapovuna na kupeleka mazao ghalani, wanategemea malipo mara moja kwa sababu changamoto zao ni kusuluhisha madeni, mikopo, ada za watoto, na huduma za afya. Hata hivyo, wakulima hawa wanaona kama wanakopesha mazao yao kutokana na kucheleweshwa malipo, hali inayotokana na ukosefu wa imani."

‎Amesema zaidi kuwa, "Kazi kubwa ambayo mnafanya ni jema katika kumkomboa Mtanzania hasa mkulima mdogo kupitia mfumo wa stakabadhi za ghala. Umeongeza ushindani, umeongeza uwazi, na umefanikiwa kuhakikisha kwamba tunalinda ubora wa mazao yetu."

‎Aidha, amesisitiza umuhimu wa ushirikiano na uwajibikaji katika utekelezaji wa mfumo huo kwa kusema, "Hatuwezi kufikia malengo kama hatuta lazimisha masoko yetu ambayo kimsingi ndiyo yanatumika kama ulinzi kwa wakulima wetu. Ni lazima kila mmoja ahakikishe tunabadilisha mind set ya Watanzania kuhusu suala zima la stakabadhi za ghala."

‎Mhe. Londo pia amewataka watumishi wa stakabadhi za ghala kusimamia ushirikiano wa karibu na sekta binafsi, akibainisha kuwa, "Hatuwezi kufanikisha bila ushiriki wa sekta binafsi katika utekelezaji wa shughuli za kila siku. Ni lazima tutaidentify stakeholders na kuwaratibu ili kufanikisha majukumu yetu."

‎Ameongeza kuwa, "Kama tukisubiri watumishi wa kutosha, hatutaweza kusimamia vizuri katika ngazi za halmashauri na usimamizi utakuwa hafifu."

‎Mhe. Denis Londo amehitimisha kwa kusema, "Na sisi tuna bahati kuwa tunatumikia nchi yetu na kuitendea haki Serikali yetu. Tutende haki Rais wetu. Kila mmoja akitimiza wajibu wake, tutafanikiwa."

‎Awali akizungumza Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala, Asangye Bangu,  amesema kuwa mfumo wa stakabadhi za ghala umeleta mafanikio makubwa katika miaka ishirini, ikiwemo kuboresha bei, kuongeza uzalishaji na ubora wa bidhaa. 

Aidha, amebainisha kuwa bidhaa kumi na nane sasa zinatekelezwa kupitia mfumo huu na mpango wa kuongeza bidhaa zisizo za kilimo kama mifugo, uvuvi, na madini unatekelezwa.

‎Aidha, amebainisha kuwa maadhimisho ya miaka ishirini yatafanyika mwezi wa 4,2026 , ambapo watashirikisha wadau waliokuwa wakifanya kazi pamoja na kuwapa elimu wanafunzi na wakulima kuhusu mfumo huo. 







Katika kuenzi siku ya kuzaliwa Rais, wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji (OR-MU), Mhe. Dkt. Pius Chaya, ameshiriki zoezi la upandaji miti katika Makao Makuu ya Ofisi hiyo, Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma.

Zoezi hilo ambalo limefanyika leo tarehe 27 Januari 2026 linaungana na jitihada za kitaifa zinazoendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali nchini kwa lengo la kuongeza uoto wa asili na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

“Natoa wito kwa wengine kuunga mkono juhudi za Mhe. Rais kwa kupanda miti ya kutosha katika mazingira yetu”. Amesema Dkt. Chaya.

Dkt. Chaya ameongeza kuwa, nchi zetu zinaathiliwa sana na matatizo ya ukame, na kukosekana kwa mvua, hivyo kupitia kampeni ya Mhe. Rais ya kuhamasisha upandaji miti ni hatua nzuri ambayo itaenda kuzitatua changamoto hizo.

Aidha, Mhe. Naibu Waziri, aliwaongoza wafanyakazi wa Ofisi hiyo kukata keki ikiwa ni Ishara ya kuadhimisha siku ya kuzaliwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, wakithamini na kutambua mchango wake katika kuleta maendeleo ya Taifa.

Sambamba na hilo, Mhe. Naibu Waziri alitumia fursa hiyo, kukagua jengo la Wizara linaloendelea kujengwa katika Mji wa Serikali Mtumba ambapo ujenzi wake umefikia asilimia zaidi ya 80 ya utekelezaji, Mhe. Dkt. Chaya amemwelekeza Mkandarasi kukamilisha na kukabidhi jengo hilo kwa mujibu wa mkataba.

Top News