Na Janeth Raphael-MichuziTv

Tume ya Uchunguzi: Ghasia za Uchaguzi Mkuu 2025 Zilipangwa, Zikafadhiliwa na Kuratibiwa na Watu Wenye Mafunzo

Tume ya kuchunguza matukio ya uvunjifu wa amani yaliyotokea wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, imebaini kuwa ghasia hizo zilikuwa zimepangwa kwa makusudi, kuratibiwa kwa umakini na kufadhiliwa na watu waliopata mafunzo maalum.

Akitoa taarifa ya Tume hiyo kwa Rais wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo Alhamisi Aprili 23, 2026, Mwenyekiti wa Tume hiyo ambaye ni Jaji Mkuu Mstaafu, Mohamed Othman Chande, amesema uchunguzi umebaini kuwepo kwa mtandao ulioratibu matukio hayo katika maeneo mbalimbali nchini.

Kwa mujibu wa Tume, wahusika walitumia mbinu mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuwashawishi vijana na watu waliokuwa katika mazingira magumu ya maisha, ikiwemo wasio na ajira na waliokata tamaa, ili kuwashirikisha katika maandamano na ghasia hizo.

Aidha, imeelezwa kuwa baadhi ya vijana walitumiwa kupitia maeneo ya vyuo, masoko na maeneo yenye mikusanyiko mikubwa ya watu, ambapo walikuwa wakishawishiwa na kuandikishwa kushiriki katika vurugu hizo.

Tume hiyo imesema watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi, waendesha pikipiki pamoja na wajasiriamali wadogo walieleza kupewa fedha kati ya Shilingi 10,000 hadi 50,000 kama motisha ya kushiriki, huku wakiahidiwa ajira na maisha bora.

Kwa mujibu wa ushahidi uliokusanywa, kati ya tarehe 12 Oktoba hadi 28 Oktoba 2025, washiriki wengi waliwekwa pamoja, wakapewa mafunzo na kuandaliwa kwa ajili ya kuanzisha na kushiriki ghasia zilizotokea siku ya uchaguzi.

Jaji Chande ameongeza kuwa uchunguzi umebaini kuwa waliokuwa wakishawishiwa na kuandaliwa ndiyo walioonekana kushiriki kwa wingi katika vurugu hizo, huku waratibu wakuu wakibaki nyuma na kuepuka maeneo ya tukio.

Hali hiyo, kwa mujibu wa Tume, ilisababisha changamoto katika kuwabaini na kuwakamata wahusika wakuu, ambapo mara nyingi walikamatwa zaidi wananchi wa kawaida waliokuwa wafuata mkumbo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Ripoti ya Tume ya Rais ya Kuchunguza Matukio ya Uvunjifu wa Amani wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 2025, kutoka kwa Mwenyekiti wa Tume hiyo, Jaji Mkuu Mstaafu Mhe. Mohamed Chande Othman, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 23 Aprili, 2026.





-Wakaguzi wakuu wa migodi watakiwa kupewa fursa zaidi kuimarisha usalama na utunzaji wa mazingira


📍KAHAMA

Serikali imeendelea kusisitiza umuhimu wa kuwawezesha Wakaguzi Wakuu wa Migodi pamoja na wachimbaji wadogo nchini ili kuimarisha usalama kazini, kulinda mazingira na kuongeza mchango wa sekta ya madini katika ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Wito huo umetolewa leo Aprili 23, 2026 wilayani Kahama, mkoani Shinyanga na Mkurugenzi wa Huduma za Leseni wa Tume ya Madini, Mhandisi Aziza Swedi, alipokuwa akifungua mafunzo kwa mameneja na Wakaguzi Wakuu wa Migodi ya uchimbaji mdogo kwa niaba ya Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhani Lwamo.

Mafunzo hayo yanawakutanisha washiriki kutoka mikoa ya kimadini ya Kahama, Mbogwe na Shinyanga yakilenga kuimarisha uelewa wa kitaalam, usimamizi bora wa migodi, uzingatiaji wa sheria na kanuni pamoja na kukuza uchimbaji salama na endelevu.

Akizungumza wakati wa ufunguzi huo, Mhandisi Swedi amesema Wakaguzi Wakuu wa Migodi wanapaswa kupewa ushirikiano na mazingira wezeshi ili waweze kutekeleza majukumu yao kikamilifu, hatua itakayosaidia kuzuia ajali migodini, kulinda afya za wachimbaji na kuhifadhi mazingira yanayozunguka maeneo ya uchimbaji.

Amesema mafanikio ya jitihada za Serikali katika kuwawezesha wachimbaji wadogo yanategemea ushirikiano wa wadau wote, hususan mameneja na wakaguzi wa migodi ambao ni nguzo muhimu katika kusimamia uzingatiaji wa sheria, kanuni na viwango vya usalama.

“Serikali inalenga kuhakikisha shughuli za uchimbaji zinaendelea kuchangia maendeleo ya Taifa huku zikifanyika kwa njia salama zisizoathiri mazingira, afya za wachimbaji na ustawi wa jamii,” amesema.

Aidha, amesema kupitia usimamizi madhubuti, nchi inaweza kufikia azma ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuongeza mchango wa sekta ya madini katika Pato la Taifa kutoka asilimia 10 ya sasa hadi asilimia 12.5 ifikapo mwaka 2030.

Ameeleza kuwa wachimbaji wadogo tayari wanachangia takribani asilimia 40 ya mapato yatokanayo na shughuli za madini, hali inayoonesha umuhimu wao katika uchumi wa Taifa, huku akiwataka wamiliki wa migodi kuhakikisha taarifa za uzalishaji na kumbukumbu muhimu zinatunzwa ipasavyo ili Serikali ipate mapato stahiki kwa wakati.

Mhandisi Swedi pia ameonya kuhusu athari za uchimbaji usiozingatia taratibu, akitaja matumizi holela ya kemikali hatarishi kama zebaki na sayanaidi pamoja na vumbi la silica kuwa chanzo cha magonjwa hatari ikiwemo silicosis, kifua kikuu na saratani.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Migodi na Mazingira kutoka Tume ya Madini, Mhandisi Hamisi Kamando, amesema Wakaguzi Wakuu wa Migodi wanapaswa kuwasilisha taarifa za ukaguzi mara kwa mara ili kuiwezesha Serikali kubaini mapema vihatarishi vinavyoweza kusababisha ajali na kuchukua hatua za kinga kwa wakati.

Amesema bado kuna changamoto katika baadhi ya maeneo ya migodi ikiwemo ukiukwaji wa sheria, ukosefu wa kumbukumbu sahihi za uzalishaji, ukwepaji wa kodi na utoroshaji wa madini, hivyo mafunzo hayo yanalenga kuwajengea washiriki uwezo wa kuwa mabalozi wa uzingatiaji wa sheria na taratibu za sekta hiyo.

“Tunataka kuona wachimbaji wanaingia migodini salama na kurejea majumbani mwao salama kila siku. Uhai wa binadamu una thamani kubwa kuliko madini,” amesema Mhandisi Kamando.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji Wadogo wa Madini Mkoa wa Shinyanga (SHIREMA), Hamza Tandiko, amesisitiza umuhimu wa weledi kwa wachimbaji na utoaji wa taarifa sahihi za shughuli za uchimbaji, huku akipongeza mchango wa wakaguzi katika kupunguza ajali na madhara migodini.












-Ataka kazi zikamilike ifikapo Mei 2027.

Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) Mhandisi Victor Seff amefanya ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa barabara zinazoingia katika uwanja utakaotumika kwa mashindano ya AFCON jijini Arusha.

Mhandisi Seff amesema kwamba ziara hiyo imelenga kujionea hatua za utekelezaji wa mradi wa barabara zenye urefu wa kilomita 21.4 ambapo kazi tayari zimeanza katika sehemu ya barabara ya Essuri.

Amesema serikali imejipanga kuhakikisha miundombinu hiyo inakamilika kwa wakati na kuongeza kuwa maeneo ambayo bado hayajaanza yanasubiri kukamilisha taratibu za fidia kwa wananchi watakaoathiriwa na mradi huo huku mkakati ukiwa ni kuendelea kuzungumza nao ili kutoa ushirikiano na kuruhusu kazi ziendelee bila vikwazo.

“Lengo la Serikali ni kuhakikisha barabara hizi zinakamilika ifikapo Mei mwaka 2027 ili ziwe tayari kabla ya mashindano ya AFCON,” amesema Mhandisi Seff.

Aidha, amesema mradi huo unatekelezwa kwa utaratibu wa Sanifu na Jenga (Design and Build) unaotumika pale ambapo muda ni mchache huku hatua zote za ununuzi tayari zikikamilika.

Ameeleza kuwa TARURA itaendelea kufanya ufuatiliaji wa karibu kuhakikisha mkandarasi anakamilisha kazi kwa wakati na kwa viwango vinavyotakiwa sanjari na ratiba ya mashindano hayo makubwa ya Mataifa ya  Afrika.

Ameongeza kuwa kwa sasa Mkandarasi M/s China Railway Construction Engineering Group tayari ameanza kazi ambapo ameanza na barabara ya Essuri yenye urefu wa kilomita 2.45 pia kutajengwa daraja lenye urefu wa mita 100.

Kwa upande wa barabara ya Lendita yenye kilomita 2.75, Mhandisi Seff amesema barabara hiyo itajengwa pamoja na daraja katika awamu ya pili ya mradi huku barabara hiyo ikitarajiwa kuwa ya njia nne.

Ameongeza kusema pia barabara ya Mateves yenye kilomita 6.5 itajengwa kwa sehemu mbili ambapo kilomita 5.5 zitakuwa njia mbili na kilomita 1 itakuwa njia nne.

Mtendaji Mkuu huyo amesema kukamilika kwa mradi huo kutaleta mafanikio makubwa kwa Taasisi hiyo kwa kupata uzoefu wa kusimamia miradi ya  Sanifu na Jenga, huku wananchi wakinufaika kwa kuondokana na changamoto ya miundombinu  katika maeneo hayo.

Vilevile, amesema wakazi wa maeneo yanayozunguka mradi huo watapewa kipaumbele cha ajira na amewataka vijana kujitokeza  kupata ajira na kutumia fursa hiyo kujiongezea kipato pamoja na  uzoefu wa kazi.

Kwa upande mwingine amewataka wasimamizi wa mradi huo kusimamia kwa karibu utekelezaji wake kwani mashindano hayo yanatarajiwa kuanza Julai mwakani.

Naye, Mhandisi Mshauri kutoka  kampuni ya M/s Afrisa Construction Engineering Group Bw. Idephonce Karol amesema mradi huo ulianza rasmi  tarehe 1 Aprili, 2026 na kwa sasa hatua za awali zinaendelea vizuri.

Amesema tayari wamehamasisha timu ya wataalamu, kufanya upimaji wa maeneo yote matatu ya barabara, uchunguzi wa udongo, tathmini ya vifaa vya ujenzi pamoja na kusafisha sehemu ya barabara ya Essuri urefu wa kilomita 1.8.

“Tumejipanga kikamilifu na tunafahamu umuhimu wa mradi huu hivyo tutafanya kazi usiku na mchana ili kuhakikisha unakamilika kwa wakati,” amesema Karol.






Na Janeth Raphael MichuziTv

Tume ya Uchunguzi wa Matukio ya Uvunjifu wa Amani yaliyotokea wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, imesema jumla ya watu 518 walipoteza maisha kutokana na ghasia zilizojitokeza siku ya uchaguzi huo.

Akiwasilisha ripoti ya Tume hiyo leo Ikulu jijini Dar es Salaam leo, Mwenyekiti wake Jaji Mkuu Mstaafu Mohamed Othman Chande amesema vifo hivyo vilitokea katika maeneo mbalimbali nchini, huku Mkoa wa Dar es Salaam ukiongoza kwa idadi kubwa zaidi ya wahanga.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, Dar es Salaam ilirekodi vifo 182, ikifuatiwa na Mwanza (90), Mbeya (80), Arusha (53), na mikoa mingine ikiwa na jumla ya vifo 113.

Jaji Chande amesema kati ya watu 518 waliofariki, wanaume ni 490 sawa na asilimia 94.6, huku wanawake wakiwa 28 (asilimia 5.4). Aidha, alibainisha kuwa sehemu kubwa ya vifo hivyo vilikuwa vya aina isiyo ya kawaida (unnatural deaths).

“Tathmini ya Tume ni kuwa jumla ya vifo vilivyotokana na ghasia za Uchaguzi Mkuu ni 518. Kati ya hivyo, 21 walikuwa watoto,” alisema Jaji Chande.

Kwa mujibu wa takwimu hizo, watoto waliofariki ni pamoja na 15 wenye umri kati ya miaka 15–17, wanne wenye miaka 7–10, na wawili chini ya miaka mitano.

Ripoti hiyo pia imeeleza kuwa vifo 502 (asilimia 96.9) vilikuwa vya raia, huku 16 (asilimia 3.1) wakiwa ni maafisa na askari wa vyombo vya ulinzi na usalama.

Kuhusu mazingira ya vifo hivyo, Tume imesema watu 373 walifikishwa hospitalini wakiwa tayari wamefariki dunia, 121 walifariki wakiwa wanapatiwa matibabu, na miili 24 haikuwa na taarifa kutoka vituo vya huduma za afya.

Aidha, kati ya miili yote 518, miili 480 sawa na asilimia 92.7 ilitambuliwa na kuchukuliwa na ndugu na familia zao.

Ripoti hiyo ni sehemu ya uchunguzi mpana uliofanywa kubaini chanzo na athari za ghasia zilizotokea wakati na baada ya uchaguzi huo.







 

Mr. Saviour Chibiya (third from right), Absa Bank East Africa Regional Executive, engaged in a strategic discussion with Mr. Rumisho Shikonyi (third from right), Country Manager of Watu Credit Tanzania, during his courtesy visit to the asset finance company in Dar es Salaam yesterday. He was accompanied by Absa Bank Tanzania Managing Director, Mr. Obedi Laiser (second from right), along with members of the executive committee. The engagement centered on strengthening collaboration, unlocking new opportunities, and driving sustainable growth across the region. Mr. Chibiya is currently in Tanzania on his official working visit.
Obedi Laiser (third from left), Managing Director of Absa Bank Tanzania, engages in conversation with Mr. Rumisho Shikonyi (right), Country Manager of Watu Credit Tanzania, during a courtesy visit by Mr. Saviour Chibiya (second from left), Absa’s East Africa Regional Executive, to the asset finance company in Dar es Salaam yesterday. The meeting focused on strengthening collaboration, unlocking new opportunities, and driving sustainable growth across the region. Mr. Chibiya is currently in Tanzania on his official working visit.
Mr. Saviour Chibiya (left), Absa Bank East Africa Regional Executive, listens attentively to Mr. Rumisho Shikonyi (right), Country Manager of Watu Credit Tanzania, during his courtesy visit to the asset finance company in Dar es Salaam yesterday. He was accompanied by Absa Bank Tanzania Managing Director, Mr. Obedi Laiser (second from left), along with members of the executive committee. The engagement centered on strengthening collaboration, unlocking new opportunities, and driving sustainable growth across the region. Mr. Chibiya is currently in Tanzania on his official working visit.

Benki ya NMB imesema uwekezaji wake katika mifumo ya kidijitali ya ukusanyaji wa mapato umeisaidia Serikali kukusanya zaidi ya Sh trilioni 9.8 kupitia majukwaa yake tangu mwaka 2018.

 Mafanikio hayo yalielezwa Arusha wakati wa mkutano mkuu maalum wa uchaguzi wa viongozi wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT).

Akizungumza katika mkutano huo, Mkurugenzi wa Uhusiano wa Wawekezaji, Uendelevu na Mawasiliano wa NMB, Innocent Yonazi, alisema hatua hiyo imetokana na ushirikiano wa karibu kati ya benki hiyo na taasisi za umma katika kuboresha usimamizi wa mapato ya Serikali. 

Alisema NMB imewekeza katika mifumo ya kisasa ya malipo inayorahisisha malipo ya Serikali kwa wananchi, wafanyabiashara na taasisi mbalimbali kwa uwazi, urahisi na ufanisi mkubwa, huku ikisaidia kupunguza mianya ya upotevu wa mapato.

Yonazi alisema pia benki hiyo imeendelea kupanua wigo wa ujumuishaji wa kifedha nchini kwa kufikia zaidi ya vijiji 3,000 na kufungua zaidi ya akaunti milioni mbili mpya. Aliongeza kuwa thamani ya mali za NMB imeongezeka kutoka Sh trilioni 7.1 mwaka 2020 hadi Sh trilioni 17.2 mwaka 2025, sawa na ongezeko la asilimia 142, huku faida kabla ya kodi ikifikia Sh trilioni 1.1.

Akifungua mkutano huo Aprili 22, 2026, Waziri Mkuu Dk. Mwigulu Lameck Nchemba aliwataka viongozi wa serikali za mitaa kuikuza sekta binafsi ili ichochee zaidi ukuaji wa uchumi na kusaidia kufikiwa kwa Dira ya Taifa ya 2050 ya uchumi wa dola trilioni 1. 

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa ALAT, Murshid Ngeze, alisema mkutano huo umewakutanisha zaidi ya wajumbe 400 kwa ajili ya kuchagua viongozi wapya watakaoiongoza jumuiya hiyo kwa kipindi cha miaka mitano ijayo.

Mkurugenzi wa Uhusiano wa Wawekezaji, Uendelevu na Mawasiliano wa Benki ya NMB, Innocent Yonazi, akizungumzia mafanikio ya taasisi hiyo mbele ya Waziri Mkuu Dr Mwigulu Nchemba katika mkutano mkuu maalum wa uchaguzi wa viongozi wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) unaofanyika Arusha.
Meneja kanda ya kati wa Benki ya NMB Janeth Shango akiteta jambo na Makamu Mwenyekiti wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) Sima Constantine Sima katika mkutano mkuu maalum wa uchaguzi wa viongozi wa unaofanyika Arusha.Kulia ni Josephine Kulwa Meneja  Mwandamizi wa biashara za serikali.


 

Mkuu wa kanda ya kati Vodacom Tanzania Plc Chiha Nchimbi (katikati) akifafanua kuhusu huduma ya afya mkopo kwa Naibu Waziri wa afya Dk Florence Samizi aliyetembelea banda la Afya mkopo katika kongamano la wadau wa sekta ya afya binafsi linaloendelea jijini Dodoma. 

Vodacom Tanzania Plc kwa kushirikiana na PharmAccess Foundation kupitia Medical Credit Fund wanatoa huduma ya mikopo kwa watoa huduma binafsi wa sekta ya afya Kupitia mfumo wa LIPA NAMBA, watoa huduma wanapata mikopo kwa haraka, kwa urahisi na kwa masharti nafuu ili kupanua huduma, kuboresha miundombinu na kukuza biashara zao. 

Kushoto kwake ni Dk Heri Marwa Mkurugenzi wa PharmAccess Foundation na kulia ni Maula Mafuru Meneja mauzo wa M-Pesa kanda ya kati 






-Asema kuna miradi inakwama utekelezaji sababu ya migawanyiko

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka viongozi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa waepuke migogoro na mizozo kwa sababu kuna miradi inakwama utekelezaji kutokana na migawanyiko.

“Twendeni tukatimize wajibu wetu, tuache migawanyiko kwa sababu hayo si matarajio ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan,” amesisitiza wakati akizungumza na washiriki wa Mkutano Mkuu Maalum wa Uchaguzi wa Viongozi wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) katika ukumbi wa mikutano wa AICC, jijini Arusha.

Ametoa wito huo leo jioni (Jumatano, Aprili 22, 2026) wakati akifungua mkutano huo wa siku mbili ulioanza leo na kusisitiza kuwa waangalie uwezekano wa kuondoa uchaguzi wa Makamu Mwenyekiti ambao hivi sasa unafanyika kila mwaka.

“Tuepuke migogoro, Waheshimiwa Mameya, Madiwani na Wenyeviti; kuna baadhi ya maeneo tunachelewa kutekeleza miradi ya maendeleo kwa sababu ya migogoro inayotengeneza migawanyiko.”

“Ondoeni utaratibu wa kuchagua Makamu Mweneyekiti kila mwaka kwani jambo hili linaleta makovu. Nimeshamuagiza Waziri wa TAMISEMI amuandikie Mwanasheria Mkuu wa Serikali kama ni sheria ifutwe, kama ni kanuni ibadilishwe, lakini kama mkutano huu una mamlaka, utaratibu wa kuchagua Makamu Mwenyekiti kila mwaka ufutwe,” amesisitiza.

Waziri Mkuu amesema utaratibu wa sasa unawanyima fursa viongozi walioko madarakani kujielekeza kwenye masuala ya kuwaletea maendeleo wananchi na badala yake wanajikuta kwenye harakati za kugawana vyeo.

“Wenyeviti wanajikuta wanaongoza watu waliogawanyika na hili halileti tija. Hivi sasa walioko madarakani bado wanajifunza kazi, tayari wengine wameshaanza kampeni kuwania nafasi zao,” amesisitiza.

Aidha, aliwataka viongozi watakaochaguliwa kesho wahakikishe wanakuwa chachu ya maendeleo na kusimamia maslahi ya wananchi kwa vitendo na kuongeza: “Kwa viongozi mtakaochaguliwa, mhakikishe mnakwenda kusaidia Jumuiya yetu na maslahi ya wananchi, muwe viongozi wanaopinga rushwa kwa vitendo. Mhakikishe mnakuwa daraja la kuleta maendeleo kwa wananchi na kuitafsiri Dira ya 2050.”

Wakati huohuo, Waziri Mkuu amesema sekta binafsi ina nafasi kubwa katika kufanikisha Dira ya Taifa 2050, akiwataka viongozi wa Halmashauri wawe wasimamizi na walezi wa mazingira rafiki ya uwekezaji.

“Katika DIRA 20250, sekta binafsi imepewa asilimia 70 za kutoa mchango. Wakurugenzi na Wenyeviti wa Halmashauri mkawe walezi wa sekta binafsi. Mkitanguliza kulea sekta binafsi mtakuza mapato. Mkitanguliza mapato mtaua sekta binafsi. Sekta binafsi tunaitegemea sana katika kutengeneza ajira kwa akinamama na vijana,” alisisitiza.

Aidha, aliwataka viongozi hao kutojihisi dhaifu katika utekelezaji wa majukumu yao, akisisitiza kuwa Serikali inatambua mchango wao mkubwa licha ya changamoto chache zinazojitokeza.

“Msipate unyonge, Mheshimiwa Rais anatambua kazi kubwa ya usimamizi wa miradi ya maendeleo mnayoifanya; ni kweli kuna baadhi ya wachache wanaotuangusha, lakini wengi wenu mnafanya kazi vizuri sana,” alisisitiza.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu aliwahakikishia wajumbe wa mkutano kuwa Serikali inaendelea kulifanyia kazi suala la kuboresha maslahi ya madiwani kama ambavyo liliwasilishwa na Mwenyekiti wa ALAT anayemaliza muda wake, Bw. Murshid Ngeze.

“Niwahakikishie Mheshimiwa Rais anatambua kazi kubwa madiwani mnayoifanya; jambo lenu linajitosheleza na linaeleweka, Serikali inaendelea kulifanyia kazi,” amesema.







Josephine Majura, WF, Dodoma


Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), amesema kuwa Serikali inatekeleza mkakati wa Mfumo wa Kodi ya Makadirio (Presumptive Tax Scheme) ili kuwahamasisha walipakodi wadogo wasiokuwa na kumbukumbu sahihi za mapato kusajili biashara zao na kuanza kulipa kodi kwa hiari.

Ameyasema hayo bungeni jijini Dodoma, wakati akijibu swali la Mbunge wa Busokelo Mhe. Lutengano Mwalwiba, aliyetaka kujua mpango wa Serikali wa kuweka vivutio maalum vya kikodi kwa Vijana wanaoanza biashara ili kuchochea ajira na kukuza uchumi.

Mhandisi Munde, alisema kuwa, mkakati huo unaolenga kuwasaidia walipakodi wadogo wasiokuwa na kumbukumbu sahihi za mapato au vitabu vya hesabu, kwa kuwa masharti yake ni mepesi na yanatabirika.

“Serikali pia imeanzisha utaratibu wa kipindi cha neema (grace period) kinachowaruhusu wafanyabiashara wapya kufanya biashara bila kulipa kodi kwa muda wa miezi sita tangu kuanza shughuli zao ili kutoa nafasi kwa wajasiriamali kukuza biashara zao na kujiimarisha kabla ya kuanza kulipa kodi”, alisema Mhandisi Munde.

Alisema kuwa Serikali inatambua umuhimu wa kutoa vivutio maalum vya kikodi kwa vijana ili kuchochea uanzishaji wa biashara na ajira, ikiwemo msamaha wa kodi na viwango pungufu, huku ikiendelea kufanya tathmini ya athari zake ili kuhakikisha usawa, ufanisi wa sera, na uendelevu wa mapato ya Serikali.

Kupitia Sheria ya Fedha ya Mwaka 2023 na Maboresho ya Mwaka 2024, Serikali pia imetoa ahirisho la kodi ya mapato (Corporate Income Tax) kwa kipindi cha miezi sita ya mwanzo kwa biashara mpya (start-ups), hatua inayolenga kusaidia biashara changa kukua na hatimaye kuwa na walipakodi wakubwa na endelevu.



Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania(TCAA), kama sehemu ya kurudisha kwa jamii, imetoa msaada katika kituo cha kulelea watoto cha Tupendane kilichopo jijini Dodoma huku ikitoa wito kwa wadau mbalimbali kuendelea kuwa na moyo wa kusaidia jamii, hususan vituo vya kulelea watoto.

Akizungumza wakati wa kupokea msaada huo, Subira Yasini, mlezi wa Kituo cha Tupendane, ameishukuru TCAA kwa kuguswa na mahitaji ya kituo hicho na kueleza kuwa msaada huo utasaidia kuboresha huduma na mazingira ya malezi kwa watoto waliopo kituoni. Alisema hatua hiyo inaonesha mshikamano na kujali ustawi wa makundi yenye uhitaji maalum katika jamii.

Awali, Bi. Subira alieleza changamoto mbalimbali zinazowakabili, ikiwa ni pamoja na ukosefu wa eneo la kudumu la makazi ya watoto hao, kwani kwa sasa wanatumia eneo la mtu aliyewapatia hifadhi ya muda.

Kituo hicho cha Tupendane kina jumla ya watoto 35, ambapo 22 kati yao wanasoma katika ngazi mbalimbali kuanzia elimu ya msingi hadi sekondari.

Kwa upande wake, Ally Changwila, Meneja Uhusiano wa Mamlaka hiyo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TCAA Bw. Salim Msangi, alisema kuwa Mamlaka hiyo inaendelea kuimarisha mahusiano chanya na jamii kwa kushiriki katika shughuli za maendeleo ya kijamii. Ameeleza kuwa msaada uliotolewa katika kituo hicho unaakisi dhamira ya TCAA ya kuchangia ustawi wa jamii sambamba na majukumu yake ya msingi katika usimamizi wa usafiri wa anga.

Aidha, aliongeza kuwa Mkurugenzi Mkuu wa TCAA ameelekeza kuwa, kutokana na umuhimu wa kurejesha kwa jamii na kusaidia wenye uhitaji, kila robo ya mwaka wa fedha angalau TCAA itoe msaada katika mojawapo ya vituo vyake vya kazi nchini. TCAA ina vituo 16 nchi nzima vinavyotoa huduma ya uongozaji ndege.

Kwa upande wake, Aswile Kamendu, Meneja wa TCAA Kituo cha Dodoma, alisema kuwa TCAA itaendelea kushirikiana na Taasisi na vituo mbalimbali vya kijamii katika mkoa wa Dodoma na mikoa mingine ili kusaidia juhudi za Serikali na wadau wengine katika kuboresha maisha ya wananchi.

Msaada uliotolewa katika kituo hicho cha Tupendane ni pamoja na vyakula vya aina mbalimbali, sabuni, mafuta ya kupikia pamoja na vifaa vya shule ikiwemo mabegi na madaftari.
Meneja Uhusiano wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania(TCAA) Ally Changwila (wa pili kulia) aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa TCAA Bw. Salim Msangi pamoja na  Meneja wa TCAA Kituo cha Dodoma Aswile Kamendu wakiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya walezi na watoto wanaolelewa katika  kituo cha Tupendane kilichopo jijini Dodoma
Meneja Uhusiano wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania(TCAA) Ally Changwila akitoa salamu za Mkurugenzi Mkuu wa TCAA Bw. Salim Msangi wakati wa kutoa msaada katika kituo cha kulelea watoto cha Tupendane kilichopo jijini Dodoma
Meneja wa TCAA Kituo cha Dodoma Aswile Kamendu akizungumza kuhusu namna watakavyoendelea kushirikiana na Taasisi na vituo mbalimbali vya kijamii kwa kutoa misaada mbalimbali katika mkoa wa Dodoma  



Top News