Na Said Mwishehe,Michuzi TV


KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) Dk.Asha-Rose Migiroameweka wazi kuwa vurugu zilizotokeaOktoba 29 mwaka 2025 zimetia doa katikataifa la Tanzania lakini limeweza kuvukakipindi kile na kubaki kuwa Taifa moja.

Dk.Migiro ameyasema hayo alipokuwa ajibu maswali ya mtangazaji wa Crown Media Salim Kikeke aliyekuwa akifanya mahojiano maalumu na Katibu Mkuu huyo kuhusu hali ambayo Taifa limepitia baada ya vurugu za Oktoba29.

Katika swali lake Kikeke alisema kuna watu kutoka vyama vya vingine na wengine kutoka ndani ya CCM wanazungumza mambo ambayo ukiyatazama unaona kimsingi kama yanaligawa Taifa badala ya kulileta pamoja, hivyo akataka kujua msimamo wa Chama Cha Mapinduzi katika hilo

“Pamoja na kwamba wapo wanaopazasauti hizo lakini ukweli ni tumebaki kuwataifa moja, tumeendeelea kuendeshashughuli zetu za kiuchumi na kijamii bilakutetereka ndani muda mfupi,amani ilirejea,uchumi wetu bado umebaki tulivu natunajua duniani kuna vyombo vya kupima,kutathimini ukuaji wa uchumi.

Vyombo vyote vimeeleza hata baada ya kadhia ile ya Oktoba 29 uchumi wetu umebaki tulivu.

“Hii inaonesha sio tu ustahimilivu ,inaonesha tumeendeelea kuwa taifa mojatukiwa na njia moja ya kujijenga kijamii nakiuchumi lakini utaona hali hii ya umoja nautulivu haipimwi tu na sisi wa ndani au Chama Cha Mapinduzi .Tumeona baada yatukuo lile bado watu wameendelea kuwa naimani na taifa hili, wameendeelea kuonautulivu wetu umerejea.”

Akiendelea kujibu Dk.Migiro amesema Rais na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi aliwapokea wawekezaji kutoka mataifa matano.Pia taifa limepokea wafanyabiashara kutoka Urusi huku akiongeza China pia imeendelea kuwekeza.

“Nasiku za karibuni Mwakillishi Mkazi wa Kanda hii wa Benki ya Dunia alikwenda kumuaga Rais wetu baada ya kumaliza kipindi chake cha utumishi katika kanda hiina alimueleza kuwaTanzania bado inamaoteo mazuri ya kukua kwa uchumi.

“Kwahiyo siamini kama tungekuwa ni taifalililogawanyika haya yote yangetokea nawapo tumewasikia wanaosema taifalimegawanyika ,limepasuka.Chochote wanachokiona ambacho ni kiashiria cha kugawanyika au kiashiria cha mpasuko Mtanzania yeyote ambaye ana mapenzi mema na taifa letu atakuwa na sauti ya kuunganisha ,sio sauti ya kuleta mpasuko na hili linakuwa na umuhimu zaidi kwa watukama sisi viongozi .

“Nimewahi kuwa kiongozi kwa nafasi yangundogo mpaka ngazi ya Uwaziri. Kitaifanimepata heshima kubwa ya kufanya kazinyingine katika taifa letu ,nilikuwa mpaka Julai mwaka jana nilipata heshima ya kuwa Mwenyekiti wa Tume ya kitalaam ya uandishi wa Dira ya Taifa 2050 .Niheshima kubwa na ni sehemu ya uongozi ambaonilipata heshima ya kuwa nayo.

“Kwa maana hiyo ninapozungumza lazimakauli yangu iakisi dhamana na heshimaniliyopewa ya kuwa kiongozi .Sauti yangukama kiongozi au viongozi wengine wawewakijamii , dini au kisiasa. Kiongozi wakweli ni yule anayepaza sauti ya kukubalikuna kitu kilitupata lakini kusema kwamba tusiendelee kukaa kwenye kadhia hii kwa namna ya kuendeleza mpasuko,”amesema Dk.Migiro na kusisitiza hakuna mgawanyiko.

Pia amesema viongozi wanawajibu wakuhakikisha wanaendelea kwa kauli zetu navitendo vyao kushikamana kama taifa nakuimarisha umoja wetu .

Kuhusu ripoti ya Jaji Chande kuwa walibainiuwepo wa picha za akili unde ambazozilitizamwa na kuna madai pengine kunapicha zinasingiziwa akili unde ili kufichayaliyotokea Oktoba 29 na nini maoni yaCCM

Dk.Migiro amejibu kuna picha ambazo akiliunde lakini kuna picha ambazo ni za matukio ya zamani zimeunganishwa namatukio ya Oktoba 29 na tume imeelezaziko picha ambazo ni za matukio yasehemu nyingine nje ya nchi lakinizimeunganishwa.

“Sasa tume ilipokuwa inaeleza metholodojia iliyotumia ilisema \wametumia watalaam wautambuzi kutambua zile picha ni za lini ,zawapi na za wakati gani. Hayo ni masuala yakitalaam .Mimi na wewe ndugu Kikekesidhani kama tuna nafasi kubwa yakuzungumzia utalaam wa aina hii.

“Wewe mwenzangu ni mtalaam wa mambo ya habari kama hivi unavyonihoji .Mimi ninataaluma yangu ndogo ya sheria lakini sikusomea sheria ya utambuzi .Nadhani itakuwa vema na busara tukawaachia watalaam wakachambua hili na tunaamini baada ya Tume ya Upelelezi wa Jinai kumaliza kazi yake tutapata mwanga zaidi kuonesha mambo zaidi yalikuaje Oktoba 29 na baadae nini kilitokea,”amesemaDk.Migiro.


Paris, Ufaransa

Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Ufaransa, Mheshimiwa Saidi Othman Yakubu, amekutana na ujumbe wa viongozi wanawake 18 kutoka Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) waliopo nchini Ufaransa kwa ziara ya kitaaluma ya kujenga uwezo na kubadilishana uzoefu kuhusu uongozi, usimamizi wa taasisi za elimu ya juu na maendeleo ya wanawake katika nafasi za maamuzi.

Ujumbe huo unaongozwa na Dkt. Janeth Emanuel Kigoba, Mkuu wa Kitivo cha Elimu cha Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, ambaye pamoja na viongozi wengine wanashiriki programu mbalimbali za kujifunza na kutathmini mifumo bora ya uongozi na utawala katika taasisi za elimu ya juu.

Akizungumza na ujumbe huo katika Ubalozi wa Tanzania mjini Paris, Balozi Yakubu alisema imekuwa jambo la kutia moyo kuona kuwa sekta ya elimu ya juu, ambayo kwa miaka mingi imekuwa nyuma katika kufikia usawa wa kijinsia ikilinganishwa na baadhi ya sekta nyingine, sasa inaendelea kupiga hatua na kuongeza ushiriki wa wanawake katika nafasi za uongozi.

“Nimefarijika kuona idadi kubwa ya wanawake viongozi kutoka taasisi ya elimu ya juu wakishiriki katika programu za kujijengea uwezo. Elimu ndiyo msingi wa maendeleo ya jamii, hivyo ni muhimu kuona wanawake wakichukua nafasi zao stahiki katika kuongoza taasisi hizi muhimu,” alisema Balozi Yakubu.

Aliongeza kuwa vyuo vikuu vina nafasi ya kipekee katika kuandaa viongozi, wataalamu na watunga sera wa kesho, hivyo kuwepo kwa usawa wa kijinsia katika sekta hiyo kuna mchango mkubwa katika kuharakisha maendeleo ya taifa na jamii kwa ujumla.

Balozi Yakubu aliwahimiza washiriki hao kuendelea kuwa vinara wa mabadiliko katika taasisi zao kwa kuhakikisha kuwa wanawake wengi zaidi wanapata fursa za kushiriki katika uongozi, utafiti na ufundishaji.

Kwa upande wake, Dkt. Janeth Emanuel Kigoba alimshukuru Balozi Yakubu na Ubalozi wa Tanzania nchini Ufaransa kwa mapokezi na ushauri walioutoa kwa ujumbe huo, akisisitiza kuwa ziara hiyo imewapa washiriki fursa muhimu ya kujifunza uzoefu wa kimataifa unaoweza kusaidia kuimarisha utendaji na uongozi wa taasisi za elimu ya juu nchini Tanzania.

Ziara hiyo ni sehemu ya juhudi za Chuo Kikuu Huria cha Tanzania za kuimarisha uwezo wa viongozi wanawake na kukuza ushiriki wao katika nafasi za juu za uongozi, sambamba na kuchochea maendeleo ya elimu ya juu na usawa wa kijinsia nchini.



Na Mwandishi wetu Dodoma

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Dodoma imefichua kasoro nzito katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo, ikiwemo ujenzi wa mabweni ya Shule ya Sekondari ya Wasichana Kibaigwa wilayani Kongwa, ambapo baadhi ya kazi zimeonekana kutotekelezwa kwa viwango vilivyokubaliwa kwenye mikataba ya Serikali.

Katika taarifa yake kwa waandishi wa habari leo jijini Dodoma kuhusu utekelezaji wa shughuli za TAKUKURU kwa kipindi cha Januari hadi Machi 2026, Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Dodoma, Christopher Myava, amesema taasisi hiyo imebaini matumizi ya nyavu kwenye madirisha na sehemu za hewa za milango badala ya vioo vilivyotakiwa kuwekwa kwa mujibu wa ramani ya ujenzi.

Amesema uchunguzi uliofanywa na TAKUKURU umeonesha pia kuwa baadhi ya vyoo vya mabweni hayo havikuwekewa masinki kama ilivyoelekezwa kwenye michoro ya mradi, huku kuta zikikosa vigae vilivyopangwa kufungwa kwa mujibu wa makubaliano ya utekelezaji wa kazi hiyo.

“Tumebaini tofauti kubwa kati ya kazi iliyotekelezwa na maelekezo yaliyopo kwenye mkataba wa mradi. Haya ni mambo ambayo yanaathiri ubora wa miradi pamoja na thamani ya fedha za Serikali,” amesema Myava.

Mbali na dosari hizo, TAKUKURU imeeleza kuwa baadhi ya vitasa vilivyowekwa kwenye mabweni hayo havifanani na vile vilivyoainishwa kwenye mkataba, huku baadhi ya vifaa vya ujenzi ikiwemo matofali na mabati vikidaiwa kutowasilishwa maabara kwa ajili ya kupimwa ubora wake kabla ya kutumika kwenye mradi.

Katika hatua nyingine, Myava amesema taasisi hiyo imefanikiwa kubaini mapungufu katika jumla ya miradi 36 ya maendeleo yenye thamani ya zaidi ya Shilingi bilioni 156.4 kupitia operesheni za ufuatiliaji zilizofanywa katika sekta mbalimbali mkoani Dodoma.

Amesema TAKUKURU itaendelea kusimamia kwa karibu utekelezaji wa miradi yote ya maendeleo ili kuhakikisha fedha za umma zinaleta matokeo yaliyokusudiwa na wananchi wanapata huduma bora kutokana na uwekezaji wa Serikali.

“Lengo letu ni kuona miradi yote inakamilika kwa viwango vinavyostahili na kuhakikisha hakuna mianya ya ubadhirifu wa fedha za umma,” ameongeza.

Baada ya kubaini dosari hizo, wahusika wa miradi hiyo wamepewa maelekezo ya kurekebisha mapungufu yote yaliyojitokeza ili miradi hiyo iweze kukidhi viwango vya kitaalamu pamoja na thamani ya fedha zilizotumika.


NA DENIS MLOWE,NJOMBE.

MAANDALIZI ya mbio za Uchumi Parachichi Marathon yameanza kushika kasi katika mkoa wa Njombe, ikiwa ni tukio kubwa lenye lengo la kutangaza na kuhamasisha thamani ya zao la parachichi ambalo ni uti wa mgongo wa uchumi wa wakazi wa Nyanda za Juu Kusini.

Marathon hii, inayotarajiwa kufanyika tarehe 26 Julai 2026 katika viwanja vya Sabasaba Njombe Mjini, imeandaliwa kwa lengo mahususi la kuonyesha mchango wa zao la parachichi katika kujenga uchumi imara wa mkoa huo kupitia zao la Parachichi.

Kupitia mbio hizi, wakulima wadogo watapatiwa elimu kuhusu kilimo bora, namna ya kuongeza uzalishaji, pamoja na kuwezeshwa kupata pembejeo, mbolea na vifaa vya kisasa vya kilimo.

Akizungumza kuhusu maandalizi hayo, Mkurugenzi wa Speak Sports Games Promotion, Respicius Mtabingwa Kajura, ambaye pia ndiye msimamizi mkuu wa tukio hilo, amesema mbio hizo ni zaidi ya mashindano ya mbio ni jukwaa la uchumi, elimu na fursa kwa jamii.

Amesema kuwa tukio hili ni bonanza kubwa kuwahi kutokea katika mikoa ya Nyanda za Juu Kusini na linatarajiwa kuvutia washiriki kutoka maeneo mbalimbali ndani na nje ya nchi.

Kajura amesema kuwa mbio hizo zitakuwa na makundi tofauti ya washiriki wakiwemo wanaokimbia 42km, 21km, 10km na 5km. Aidha, kaulimbiu ya mwaka huu, Parachichi ni Uchumi wa Njombe na Lishe Bora ya Mwanao, inalenga kuhimiza matumizi ya parachichi kama zao la lishe na biashara.

Ametoa wito kwa wadau wa michezo, kilimo, afya na jamii kwa ujumla kuungana nao ili kufanikisha tukio hilo ambalo lina matarajio ya kuleta hamasa na utalii wa michezo katika mkoa wa Njombe.

Mkurugenzi Kajura amewakaribisha wananchi wote kutoa ushauri, mawazo na michango yao ili kuhakikisha Uchumi Parachichi Marathon inafanyika kwa ubora na mafanikio makubwa kama inavyotarajiwa.


Benki ya NMB imeendelea kuimarisha huduma kwa wafanyabiashara kupitia NMB Business Club, jukwaa linalowapa wateja elimu ya fedha, teknolojia na fursa mbalimbali za kukuza biashara zao kwa uendelevu. Semina hiyo imefanyika katika Ukumbi wa Cardinal Rugambwa, Dar es Salaam.

Akizungumza katika semina hiyo, Mwenyekiti wa NMB Business Club Mkoa wa Dar es Salaam na Mjumbe wa Bodi ya Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania (JWT), Award Mpandila, alisema jukwaa hilo limekuwa muhimu kwa kuwaunganisha wafanyabiashara na kuwajengea uwezo wa kutumia mifumo rasmi ya kifedha.

 Aliwahimiza wafanyabiashara kupitisha mauzo yao kupitia benki ili kujenga historia nzuri ya kifedha inayoweza kuwasaidia kupata huduma mbalimbali, ikiwemo mikopo.

Kwa upande wake, Meneja Mwandamizi wa Business Banking Benki ya NMB, Reynold Tony, alisema benki hiyo itaendelea kutoa bidhaa, elimu na suluhisho zinazolenga kuimarisha biashara za wateja wake. Alisema NMB inalenga kuwa mshirika wa karibu wa wafanyabiashara katika kujenga biashara imara na zinazoweza kukabiliana na mabadiliko ya soko.

Baadhi ya wafanyabiashara waliohudhuria, akiwemo Eileen Kunaga na Ally Kuburi kutoka Ilala, walisema jukwaa hilo limewasaidia kupata elimu kuhusu matumizi ya sola, usimamizi wa fedha na huduma za taasisi mbalimbali, ikiwemo TRA. Walisema maarifa hayo yanaweza kupunguza gharama za uendeshaji na kusaidia biashara kukua kwa muda mrefu.
Mwenyekiti wa NMB Business Club Mkoa wa Dar es Salaam na Mjumbe wa Bodi ya Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania (JWT), Awadhi Mpandila, akizungumza wakati wa semina ya NMB Business Club iliyofanyika Dar es Salaam. Walioketi meza kuu ni Reynold Tony Lusingu, Meneja Mwandamizi wa Idara ya Biashara Benki ya NMB; William Nkuna, Kaimu Meneja wa Kanda ya Dar es Salaam; Petro Kyando, Katibu wa NMB Business Club; na Leah Mwakang’ata, Mkuu wa Idara ya Amana za Biashara (kulia) wa Benki ya NMB.
Mkuu wa Idara ya Amana za Biashara Benki ya NMB, Leah Mwakang’ata, akizungumza wakati wa semina ya NMB Business Club iliyofanyika Dar es Salaam. Walioketi meza kuu ni Reynold Tony, Meneja Mwandamizi wa Idara ya Biashara Benki ya NMB; William Nkuna, Kaimu Meneja wa Kanda ya Dar es Salaam; Awadhi Mpandila, Mwenyekiti wa NMB Business Club Mkoa wa Dar es Salaam; na Petro Kyando, Katibu wa NMB Business Club.




















📍Wanafunzi wafurahia, wampongeza mbunge 


Na Mwandishi Wetu, Muheza

MBUNGE wa Muheza, Mhe. Hamis Mwinjuma (MwanaFA), amekagua mradi wa kisima cha maji matamu katika Shule ya Sekondari ya Kwabastola.

Shule hiyo iliopo Kata ya Makole wilayani hapa, kisima kimegharimu Shilingi milioni 12 kupitia kampuni ya Mo Maji, ikiwa ni mwendelezo wa mikakati yake ya kusogeza huduma za kijamii karibu na wapiga kura wake tangu aingie madarakani mwaka 2020.

Akizungumza mara baada ya kukagua mradi huo Leo Mei 29, 2026, Mhe. Mwinjuma alionyesha kufurahishwa na kukamilika kwake, hasa baada ya kubainika kuwa maji hayo ni matamu na hayana chumvi, jambo linaloyafanya yafae kwa matumizi ya shule na wananchi wa jirani.

"Wakati wa kampeni zangu, miongoni mwa ahadi kubwa nilizotoa ni kuhakikisha natatua kero ya dharura ya maji katika maeneo mbalimbali ya jimbo letu. Kupatikana kwa maji haya matamu hapa Kwabastola ni ushahidi kuwa tunatekeleza Ilani kwa vitendo ili kuwasaidia watoto wetu wasome kwa utulivu," alisema MwanaFA.


Mabweni na Vyoo vya Kisasa Kunusurika

Naye Ofisa Mtendaji wa Kata ya Makole,  Rose Maghembe, alimshukuru Mbunge huyo kwa uamuzi wake wa kuchimba  kisima hicho, akieleza kuwa shule hiyo ilikuwa inakabiliwa na wakati mgumu kutokana na uwepo wa majengo mapya yasiyo na maji.

"Tunashukuru sana Mbunge wetu kwa kisima hiki. Shule yetu ina mabweni ya wasichana na wavulana ambayo yana vyoo vya kisasa vya ndani ambavyo kitalamu vilikuwa haviwezi kuishi au kutumika bila maji. Upatikanaji wa maji haya sasa unakwenda kuwasaidia wanafunzi na wananchi wa jirani na shule," alisema Mtendaji huyo.

Maandalizi ya Kidato cha Tano Julai

Akiwasilisha taarifa fupi ya shule kwa niaba ya Mkuu wa Shule hiyo, Juma Rashid Mdachi, Makamu Mkuu wa Shule, Lilian Godlisten Massawe, alisema miundombinu hiyo ya maji imekuja wakati muafaka kuelekea upokeaji wa wanafunzi wapya wa kidato cha tano.

Lilian alianika takwimu zinazoonyesha kuwa shule hiyo kwa sasa ina jumla ya wanafunzi 283, wakiwemo wavulana 132 na wasichana 151 waliopo kidato cha tatu, wakisoma katika mikondo miwili kwa kila kidato chini ya usimamizi wa walimu 13.

Aliongeza kuwa, mwezi ujao wa Julai (Mwezi wa Saba), shule hiyo inatarajia kupokea kwa mara ya kwanza wanafunzi wapya wa gredi ya juu wa Kidato cha Tano (High School) kwa michepuo ya tahasusi za Sayansi (CBG) na Sanaa (HGfa), hivyo kisima hicho kitasaidia kuondoa changamoto kubwa ya ukosefu wa maji.







RAIS  mstaafu wa Awamu ya Nne Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, leo Mei 29, 2026 amekutana tena na Bi. Catherine P. Conrad Minja, aliyefanyiwa upasuaji wa moyo kwa mafanikio akiwa na umri wa miaka minne katika taasisi ya Muhimbili Orthopaedic Institute (MOI) miaka 18 iliyopita.

Wakati huo madaktari bingwa wa Moyo wa JKCI walikuwa wakitumia majengo ya MOI kabla jengo lao halijakamilika.

Mara ya kwanza wawili hao walikutana Novemba 14, 2008 wakati Dkt. Kikwete akiwa Rais alipokwenda kumjulia hali Catherine hapo MOI baada ya kufanyiwa upasuaji wa moyo mapema wiki hiyo. Wakati huo Catherine alikuwa mmoja wa wagonjwa wa mwanzo kufanyiwa upasuaji huo katika taasisi hiyo.

Miaka 18 baadaye, Catherine amekua na sasa ni mwanafunzi wa mwaka wa kwanza wa Shahada ya Udaktari katika Chuo Kikuu cha Kairuki jijini Dar es salaam.

Alifika ofisini kwa Rais Mstaafu kumsabahi na kumshukuru kwa mchango wake katika kuanzisha na kuimarisha huduma za matibabu ya magonjwa ya moyo nchini.

Dkt. Kikwete alimpongeza Catherine kwa kutimiza ndoto yake ya kusomea udaktari, jambo ambalo aliahidi kulifanya alipokuwa mtoto. Alisema amefurahishwa kumuona akiwa mwenye afya njema na akijiandaa kulitumikia taifa kupitia taaluma ya tiba.

Kwa upande wake, Catherine alisema anatamani kuwa Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo ili kuwasaidia wagonjwa wenye changamoto kama aliyowahi kupitia yeye mwenyewe, akieleza kuwa hiyo itakuwa ni moja ya njia ya kumshukuru Mungu kwa zawadi ya maisha na afya njema.


Na Seif Mangwangi, Michuzi TV, Karatu

SERIKALI imesema itaendelea kuwalinda wawekezaji wa ndani pamoja na kuunga mkono uwekezaji wowote unaofanywa na wawekezaji hao kwa lengo la kutoa huduma za kijamii.

Hayo yameelezwa leo 29 Mei 2026 na Mkuu wa Wilaya ya Karatu Lameck Karanga katika hafla ya uzinduzi wa kituo kipya ya mafuta cha Orxy kitakachokuwa kikiendeshwa chini ya kampuni ya halyaz.

DC Karanga amesema ujenzi wa kituo hicho cha mafuta ni muendelezo wa maono ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kuhakikisha wawekezaji wa ndani wanajengewa mazingira mazuri Ili waweze kufanya biashara.

Amesema Karatu ndio lango kuu la utalii hivyo ujio wa kituo hicho kutasaidia wasafirishaji kupata nishati ya mafuta kwa urahisi na uhakika kwa kuwa bidhaa za kampuni hiyo zinaaminika katika ukanda wa Afrika na duniani kote.

"Kwa niaba ya Wilaya niwapongeze sana kwa uwekezaji huu, mbali ya kutuletea kituo bora lakini mmeanza na kutengeneza mazingira hasa ya bustani nzuri hapo mbele ya kituo chenu, hii inaonyesha ni namna gani mmekuja Karatu Kwa faida," amesema na kuongeza:

"Orxy wameonyesha usafi wa mazingira nje ya kituo cha mafuta na niwaombe watu wa Benki na wenyewe waige mfano huu ni utalii mzuri na kuonyesha wilaya ya karatu ni safi na kuwa na mazingira mazuri," amesema.

Aidha DC Karanga amewataka wananchi wa mji wa Karatu kuiga mfano wa kampuni ya Halyaz kufungua taasisi kama hizo Ili kusaidia jamii kupata ajira lakini pia Serikali kupata kodi. 

Mkurugenzi wa kampuni ya Halyaz inayoendesha kituo hicho cha mafuta cha Orxy Karatu, Ally Abdulrazak amesema ujenzi wa kituo hicho ni matokeo ya maono kwamba karatu inastahili huduma bora za nishati.

Amesema aliamua kuingia ubia na kampuni ya Orxy kufungua kituo hicho cha mafuta kwa kuwa ndio kampuni ambayo imekuwa ikitoa  mafuta safi na salama kwa magari aina tofauti tofauti.

Abdulrazak amesema wateja watakaofika kupata huduma katika kituo hicho watapata huduma zenye ubora wa kimataifa kwa kuwa Wafanyakazi wake wanaujuzi wa hali ya juu lakini pia huduma zote zinaendeshwa kwa kuzingatia ubora.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Orxy Tanzania, Meneja wa fedha wa kampuni hiyo, Greyson Francis amesema uzinduzi wa kituo hicho cha mafuta cha Orxy Karatu ni sehemu ya ndoto za kampuni hiyo kuendelea kupanua huduma zake Kwa jamii.

Amesema kampuni ya Orxy imesambaa katika nchi 19 barani Afrika na hapa nchini imeshasambaa mikoa yote na hivi karibu itazindua vituo viwili vya mafuta Jijini Dar es Salaam.



 

Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Judith  Kapinga (Mb), ameliagiza Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kushirikiana kikamilifu na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) pamoja na Taasisi nyingine husika katika kushughulikia na kuondoa kero zote zinazosababishwa na mifumo ya utoaji vibali kwa shehena zinazoingia nchini.

Waziri Kapinga ametoa agizo hilo akiwa ameambatana na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Balozi Waziri Salum alipokutana na Mkurugenzi Mkuu wa TBS, Dkt. Ashura Katunzi na ujumbe wake Mei 29, 2026 katika ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam, kufuatia kuibuka kwa changamoto zilizojitokeza wakati wa kuunganisha mfumo wa TANeSW wa TRA na mfumo wa OAS wa TBS na kusababisha usumbufu kwa baadhi ya wafanyabiashara.

Aidha, Waziri Kapinga amepongeza jitihada zinazoendelea kuchukuliwa baina ya TBS pamoja na TRA katika kuunganisha mifumo ya kielektroniki ili kurahisisha taratibu na kuongeza ufanisi wa utoaji wa vibali kwa shehena za mizigo inayoingia nchini.

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali imetoa zawadi ya sh. milioni 500 kwa Timu ya Taifa ya Tanzania ya vijana chini ya miaka 17 (Serengeti Boys) kwa kufanikiwa kutinga hatua ya fainali ya mashindano hayo na kuipeperusha vyema bendera ya Tanzania kimataifa.

Dkt. Mwigulu amesema hayo leo (Ijumaa, Mei 29, 2026) ofisini kwake Mlimwa, Dodoma wakati akitoa salamu za pongezi kwa timu hiyo kufuzu hatua ya fainali kwa niaba ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Amesema Rais Samia amewapongeza wachezaji, benchi la ufundi na viongozi wote wa timu kwa mafanikio hayo makubwa ambayo yameendelea kuandika historia mpya katika sekta ya michezo nchini.

“Mheshimiwa Rais amenielekeza nitoe pongezi hizi kwa vijana wetu wa Serengeti Boys kutokana na mafanikio makubwa ya kutinga fainali na kuiwakilisha vema Tanzania katika mashindano hayo,” amesema Dkt. Mwigulu.

Waziri Mkuu amesema Serikali itatuma ndege maalum kwa ajili ya kuwafuata vijana hao watakapomaliza mashindano hayo ili kurejea nchini pamoja na kombe endapo watafanikiwa kutwaa ubingwa. “Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ametoa ndege kwa ajili ya kuwafuata vijana wetu watakapokuwa wamemaliza mashindano hayo na kurejea nao nyumbani,” amesema.

“Tunaamini huu ni mwanzo tu wa pongezi ambazo Mheshimiwa Rais ameanza kuzitoa. Tunaamini kwamba wakirejea na kombe hilo, kutakuwa na sababu zaidi ya kuwapongeza kwa mafanikio hayo makubwa.”

Waziri Mkuu amemwelekeza Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Paul Makonda na wadau wanaohusika, waendelee na uratibu wa wa safari kwa watu watakaokwenda kuwaunga mkono vijana wetu.

Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu amesema endapo Serengeti Boys watatwaa ubingwa, Serikali itawapatia kila mchezaji kiwanja kimoja katika Mji wa Suluhu New City uliopo mkoani Morogoro ikiwa ni sehemu ya kutambua mchango wao katika kuitangaza Tanzania kupitia michezo.

Waziri Mkuu pia amewahamasisha Watanzania, taasisi, mashirika na wadau mbalimbali wa michezo kuendelea kutoa msaada na motisha kwa timu hiyo kuelekea mchezo wa fainali.

“Shime shime vijana wetu, inawezekana. Tuleteeni kikombe kile, mleteeni Dkt. Samia Suluhu Hassan kikombe, tuleteeni Watanzania ushindi huo. Kwa kiwango mlichokionesha, tunaamini mna uwezo wa kutwaa ubingwa huo,” amesema.

Sambamba na hilo, Waziri Mkuu amempongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuwa kinara wa maendeleo ya michezo nchini na kuchochea mafanikio yanayoendelea kupatikana katika sekta hiyo.


-Yasema kwa mara ya kwanza Serikali ilikamata tani 29.52 za aina mpya ya dawa za kulevya aina ya Kratom

-Pia mali zenye thamani ya zaidi ya Sh.bilioni 3.3 zilizohusishwa na makosa ya dawa za kulevya zilitaifishwa.


Na Mwandishi Wetu,Michuzi TV

WAZIRI wa Nchi,Ofisi ya Waziri Mkuu(Sera,Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu) Profesa Palamagamba Kabudi ameta taarifa ya hali ya dawa za kulevya kwa mwaka 2025 ambapo inaonesha namna Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya uongozi wa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ilivyowekeza na kuweka nguvu kubwa katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya. 

Akiwasilisha taarifa hiyo leo Mei 29,2029 Bungeni Mjini Dodoma ,Profesa Kabudi amesema uwasilishaji wa taarifa hiyo ni utekelezaji wa Kifungu cha 66 cha Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Na. 5 ya Mwaka 2015, inayoiagiza Serikali kuandaa na kuwasilisha bungeni taarifa hiyo kila mwaka.

“Lengo ni kuonesha uwajibikaji wa Serikali kwa wananchi kupitia Bunge, pamoja na kutoa tathmini ya utekelezaji wa mikakati ya udhibiti wa dawa hizo kwa mwaka husika.Pia, taarifa hii inatoa nafasi kwa Bunge kutoa ushauri kwa Serikali kuhusu namna bora ya kukabiliana na tatizo la dawa za kulevya nchini.”

Amefafanua kupitia Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, vyombo vya ulinzi na usalama, wadau wa ndani na nje ya nchi pamoja na jamii kwa ujumla, serikali imepata mafanikio makubwa katika kudhibiti biashara na matumizi ya dawa za kulevya.Katika taarifa hiyo Profesa Kabudi amesema mwaka 2025, bangi iliendelea kuwa dawa ya kulevya iliyokamatwa kwa kiwango kikubwa zaidi ambapo jumla ya tani 1,017.26, zilikamatwa. 

Amefafanua hata hivyo, kiasi kilichokamatwa kilipungua kwa asilimia 55.97 ikilinganishwa na mwaka 2024.Hiyo ni kutokana na uteketezaji wa mashamba makubwa ya bangi uliofanyika mwaka 2024 na kuimarika kwa udhibiti ikiwemo utoaji elimu kwa jamii inayojihusisha na kilimo cha bangi kuhusu madhara ya kilimo cha zao hilo.

Ameongeza pia jumla ya tani 26.36 za mirungi zilikamatwa. Kiasi hicho kiliongezeka kwa asilimia 42.88 ikilinganishwa na mwaka 2024. Ongezeko hilo linaashiria kuimarika kwa operesheni za ufuatiliaji na udhibiti hususan katika maeneo ya mipaka na njia zinazotumika kusafirisha dawa hizo.

Kwa upande wa dawa za kulevya za viwandani, amesema Serikali ilifanikiwa kukamata methamphetamine kilogramu 907.18, heroin kilogramu 672.23, cocaine kilogramu 4.89, MDMA gramu 178 na MDA gramu 7.82.

Aidha, kwa mara ya kwanza, mwaka 2025 Serikali ilikamata tani 29.52 za aina mpya ya dawa za kulevya aina ya Kratom itokanayo na mmea unaoitwa Mitrogyna speciosa. “Dawa hii iliingizwa nchini kama mbolea, baada ya uchunguzi ilibainika kuwa ni dawa za kulevya.”

Amesema kuwa mafanikio hayo yametokana na kazi kubwa iliyofanywa na Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya kwa kushirikiana na vyombo vyetu vya ulinzi na usalama katika kudhibiti mitandao na njia za usafirishaji wa dawa za kulevya kupitia Nchi kavu, anga na majini.

Aidha, Serikali iliendelea kuimarisha ukaguzi katika vituo vya forodha, vyombo vya usafiri, kampuni za usafirishaji vifurushi na kwenye kampuni zinazojihusisha na biashara ya kemikali bashirifu na dawa tiba zenye asili ya kulevya kwa lengo la kudhibiti uchepushwaji. 

“Kupitia ukaguzi huo, jumla ya tani 31.76 na lita 183.500 za kemikali bashirifu pamoja na kilogramu 2.36 na mililita 160 za dawa tiba zenye asili ya kulevya zilikamatwa.”

Kuhusu makosa ya dawa za kulevya, mwaka 2025,amesema  jumla ya mashauri 1,124 yalifunguliwa katika Mahakama mbalimbali nchini. Pamoja na mashauri yaliyokuwa yakiendelea katika Mahakama mbalimbali nchini, mashauri 1,373 yalitolewa hukumu na Jamhuri ilishinda mashauri 1,058.

Aidha mali zenye thamani ya zaidi ya Tsh. bilioni 3.3 zilizohusishwa na makosa ya dawa za kulevya zilitaifishwa.Pia Serikali iliendelea kutoa huduma za tiba na utengamao kwa watu wenye uraibu wa dawa za kulevya. 

“Mwaka 2025, jumla ya watu 85,425 wenye uraibu wa dawa za kulevya walipata tiba kwenye vitengo vya afya ya akili katika hospitali za rufaa za mikoa na Kanda, kliniki za MAT na nyumba za upataji nafuu nchini.

“Elimu kuhusu madhara ya dawa za kulevya iliendelea kutolewa kwa Umma kupitia kampeni mbalimbali za uelimishaji katika jamii, taasisi za elimu na vyombo vya habari ili kuijengea jamii uelewa, maamuzi sahihi na uwezo wa kujilinda dhidi ya matumizi na biashara ya dawa za kulevya.

“Katika kuimarisha ushirikiano wa kitaifa, kikanda na kimataifa, Serikali imeendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa ndani na nje ya nchi katika kubadilishana taarifa za kiintelijensia, kujenga uwezo wa kitaasisi pamoja na kuendesha operesheni za pamoja dhidi ya mitandao ya usafirishaji na biashara ya dawa za kulevya.

“Matokeo chanya katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya yanatokana na dhamira thabiti, maono na uongozi mahiri wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwani chini ya uongozi wake amewekeza kwa kiasi kikubwa katika kufanikisha mapambano dhidi ya tatizo la dawa za kulevya Nchini.”

Pia ameipongeza Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, vyombo vyetu vya Ulinzi na Usalama, wataalamu wa afya, wadau katika mapambano na wananchi kwa ushirikiano wao uliosaidia kuyafikia mafanikio aliyoyaeleza.

“Naomba wananchi waendelea kutoa taarifa pale wanapohisi au kushuhudia viashiria vya biashara au matumizi ya dawa za kulevya kwa vyombo husika ili kuifanya nchi yetu kuwa mahali salama na huru dhidi ya matumizi na biashara dawa za kulevya.”








Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza wakati wa kikao cha kupokea Taarifa ya Sensa ya Wanyamapori iliyofanyika nchi nzima mwaka 2024 – 2025 iliyowasilishwa na Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Ashatu Kijaji, tarehe 29 Mei, 2026 Ikulu Dar es Salaam.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye kikao cha kupokea Taarifa ya Sensa ya Wanyamapori iliyofanyika nchi nzima mwaka 2024 – 2025 iliyowasilishwa na Waziri ya Maliasili na Utalii Dkt. Ashatu Kijaji kupitia Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI), tarehe 29 Mei, 2026 Ikulu Dar es Salaam.






 


Top News