Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi Mteule wa Tanzania nchini Uganda, Mhe. Balozi Meja. Jen. Marco Elisha Gaguti, mazungumzo yaliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam leo tarehe 01 Julai 2026.

Mazungumzo hayo ni kufuatia, Mhe. Balozi Gaguti, kufika kwa Makamu wa Rais kwa lengo la kumuaga akielekea katika Kituo chake cha kazi nchini Uganda, mara baada ya kuteuliwa hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.








Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda akikata utepe (kulia) akikata utepe kuashiria uzinduzi wa huduma za Next Generation Sequencing (NGS) unaoashiria enzi mpya ya tiba ya jenomiki, ukikiweka Chuo Kikuu kuwa kitovu cha kitaifa na kikanda cha sayansi ya jenomiki, uchunguzi wa kisasa wa magonjwa, utafiti na ubunifu. anayeshuhudia katikati ni Makamu Mkuu wa chuo cha MUHAS, Profesa, Appolinary Kamuhabwa.








Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali imeweka mkakati wa kuharakisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo nchini ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na miradi inakamilika kwa wakati.

Akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika Uwanja wa Sokoine, wilayani Serengeti, mkoani Mara, leo Jumatano (Julai 1, 2026), Waziri Mkuu alisema Serikali imeanza rasmi utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2025–2030, Bajeti ya Serikali ya mwaka 2026/2027 pamoja na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

"Tunaanza utekelezaji wa Ilani leo, Ilani ya 2025–2030. Tunaanza utekelezaji wa Bajeti leo ya mwaka 2026/2027, na tunaanza utekelezaji wa Dira mpya ya 2050 leo."

Waziri Mkuu alisema baadhi ya miradi ya maendeleo ilichelewa kuanza au kupungua kasi ya utekelezaji kutokana na uamuzi wa kimkakati wa Serikali wa kuelekeza rasilimali katika kukamilisha miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo Mradi wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere, Daraja la JPM na Reli ya Kisasa (SGR), ambayo sasa imeanza kuwanufaisha Watanzania.

Akizungumzia utekelezaji wa miradi ya barabara, Waziri Mkuu alisema Serikali imeweka utaratibu mpya utakaohakikisha fedha za Mfuko wa Barabara zinawafikia watekelezaji moja kwa moja ili kuondoa ucheleweshaji wa miradi.

"Kuanzia leo tarehe moja, fedha zitakazokusanywa zinazotakiwa kwenda kwenye ujenzi wa barabara, zikishakusanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania, hazitapelekwa kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali. Zitakwenda moja kwa moja kwenye Mfuko wa Barabara ili kasi ya ujenzi wa barabara isiende kwa kusuasua."

Alisema hatua hiyo itawawezesha wakandarasi waliokuwa wamesimama kurejea katika maeneo ya kazi na kuharakisha utekelezaji wa miradi mbalimbali ikiwemo ya Mkoa wa Mara.

"Nimewaelekeza wakandarasi ambao walishatoka site warudi site, kwa sababu kuanzia leo tarehe moja Mfuko wetu wa Barabara... fedha zitakwenda moja kwa moja kwenye mifuko ili wananchi wapate maendeleo yanayochochewa na miundombinu hiyo wezeshi."

Aidha, Waziri Mkuu aliwahakikishia wananchi kuwa Serikali itaendelea kusimamia utekelezaji wa ahadi zote zilizotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.

"Yale ambayo Mheshimiwa Rais aliwaahidi, amenituma niwahakikishie kuwa yatatekelezwa. Na mimi, kama wajibu niliopewa na Katiba, nitasimamia kuhakikisha maelekezo hayo ya Mheshimiwa Rais yanatekelezwa."








Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Jumatano, Julai 1, 2026, amekagua maendeleo ya ujenzi wa Jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti, lililopo mjini Mugumu, mkoani Mara, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi ya siku tano mkoani humo.

Akiwasilisha taarifa ya ujenzi huo, Msanifu Majengo wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) Mkoa wa Mara, Bw. Nicholas Jeje, alisema mradi huo unagharimu shilingi bilioni 4.5 zinazotolewa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Alisema ujenzi ulianza Aprili 10, 2025 na unatarajiwa kukamilika Aprili 9, 2028, huku utekelezaji wake ukiwa umefikia asilimia 42.

Alieleza kuwa jengo hilo litakuwa na ofisi 62, zikiwemo ofisi za Mkurugenzi wa Halmashauri na Mwenyekiti wa Halmashauri, pamoja na kumbi mbili za mikutano zenye uwezo wa kuchukua watu 50 na 110 mtawalia, hatua inayolenga kuboresha mazingira ya utoaji wa huduma kwa wananchi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mara, Kanali Evans Mtambi, alimkaribisha Waziri Mkuu mkoani humo na kusema ziara hiyo itamwezesha kutembelea wilaya zote sita, halmashauri zote tisa na majimbo yote 10 ya uchaguzi yaliyopo mkoani Mara, ambapo pamoja na mambo mengine atakagua miradi ya maendeleo na kuzungumza na wananchi.








 

Mwenyekiti wa Taifa Group na mfanyabiashara mashuhuri, Bw. Rostam Azizi, ametunukiwa Tuzo ya Juu ya Heshima ya Chemba ya Taifa ya Biashara Tanzania (TNCC) kwa kutambua mchango wake katika kukuza uwekezaji, kuunda ajira, kuboresha huduma za jamii na kuchochea maendeleo ya uchumi wa Taifa.

Tuzo hiyo ilikabidhiwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, aliyekuwa mgeni rasmi katika Kongamano la Biashara na Uwekezaji la Mwaka 2026 lililoandaliwa na TNCC katika Hoteli ya Johari Rotana, Dar es Salaam.

Akizungumza katika kongamano hilo, Dkt. Mwigulu alisema Serikali itaendelea kuimarisha mazingira ya biashara na uwekezaji kupitia maboresho ya sera, sheria, kanuni na mifumo ya utoaji huduma ili kuiwezesha sekta binafsi kuwa injini ya ukuaji wa uchumi na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

"Ajenda ya sekta binafsi ni ajenda ya Taifa. Hatuwezi kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 bila sekta binafsi yenye nguvu na inayoshirikiana kwa karibu na Serikali," amesema.

Aliongeza kuwa Serikali itaendelea kushughulikia mapendekezo ya sekta binafsi ili kuondoa vikwazo vya biashara na kuongeza ushindani wa bidhaa na huduma za Tanzania katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Kupitia uwekezaji wake katika sekta mbalimbali, Bw. Rostam Azizi amechangia uundaji wa maelfu ya ajira, kukuza uwekezaji na kuboresha huduma za jamii, hatua zilizochangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya uchumi wa Taifa.

Akizungumza baada ya kupokea tuzo hiyo, Bw. Rostam Azizi aliishukuru Serikali na TNCC kwa kutambua mchango wake, akisema tuzo hiyo ni motisha ya kuendelea kushiriki katika maendeleo ya Taifa.

"Ninapokea tuzo hii kwa heshima kubwa.

Naihusisha na juhudi za pamoja kati ya sekta binafsi na Serikali katika kujenga uchumi imara. Nawapongeza pia wadau wote waliotunukiwa tuzo mbalimbali leo kwa mchango wao katika kuimarisha sekta binafsi na kukuza uchumi wa Taifa," amesema.

Katika hafla hiyo, Waziri Mkuu pia alikabidhi tuzo mbalimbali kwa wadau wengine, akiwemo Bi. Emma Kawawa, Bw. David Mwaibula, Bw. Imani Kajula, Bw. Elibariki Mmasi na Bi. Mercy Emmanuel Sila, kwa mchango wao katika kuendeleza sekta binafsi, kuboresha mazingira ya biashara na kuimarisha shughuli za TNCC.

Na Mwandishi wetu Dodoma

Kampuni ya Alliance Life Assurance Ltd imeandika historia mpya katika sekta ya bima nchini baada ya kuzindua rasmi ofisi yake ya mauzo jijini Dodoma, hatua inayoiweka kama kampuni ya kwanza ya bima ya maisha kuwa na uwepo rasmi katika Makao Makuu ya nchi.

Uzinduzi huo umefanyika katika hafla iliyohudhuriwa na wadau mbalimbali wa sekta ya bima, akiwemo Meneja wa Mipango na Utafiti wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA), Edgar Shao, aliyemwakilisha Kamishna wa Bima, Dkt. Baghayo A. Saqware.

Akizungumza katika hafla hiyo, Shao aliipongeza Alliance Life Assurance kwa hatua hiyo, akibainisha kuwa ni ishara ya wazi ya dhamira ya kampuni hiyo katika kusogeza huduma za bima ya maisha karibu zaidi na wananchi, hususan katika kuongeza upatikanaji na uelewa wa huduma hizo nchini.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Alliance Life Assurance Ltd, Byford Mutimusakwa, amesema kufunguliwa kwa ofisi hiyo mpya ni sehemu ya mkakati mpana wa kampuni ya kupanua huduma zake nchini, pamoja na kuleta suluhisho bunifu za bima ya maisha zinazolenga kuwasaidia Watanzania kujenga usalama wa kifedha kwa sasa na baadaye.

Mutimusakwa alibainisha kuwa uwepo wa ofisi hiyo Dodoma utarahisisha upatikanaji wa huduma kwa wateja wa Mkoa wa Dodoma na mikoa jirani, sambamba na kuboresha utoaji wa huduma za ushauri wa kifedha na bima.

Ofisi hiyo mpya iko katika Ghorofa ya Kwanza ya Jengo la Kisangani, Barabara ya Majengo, jijini Dodoma, na inatarajiwa kuwa kitovu muhimu cha huduma za bima ya maisha kwa wananchi wa eneo hilo na maeneo ya jirani.

Aidha, kampuni hiyo imewahimiza wananchi kujitokeza katika ofisi hiyo mpya kupata elimu na ushauri wa kitaalamu kuhusu huduma mbalimbali za bima ya maisha zinazolenga kulinda mustakabali wa kifedha wa familia na jamii kwa ujumla.











 Dar es Salaam, 1 Julai 2026 Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) inapenda kuufahamisha Umma wa Watanzania kuwa tarehe 30 Juni 2026, imekabidhi Serikalini mchango wa TZS 61,053,535,363 ikiwa ni fedha za makusanyo yake katika kuunga mkono jitihada za Serikali ya Jamuhuriy a Muungano wa Tanzania ya kuleta maendeleo kwa wananchi. 

Mchango huo ulikabidhiwa kwa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, katika hafla ya upokeaji wa gawio na michango ya Taasisi za Umma iliyofanyika Ikulu, Dar es Salaam. 

Katika hafla hiyo, NIDA pia ilipata heshima ya kutunukiwa tuzo baada ya kushika nafasi ya pili miongoni mwa Taasisi zilizofanya vizuri katika kuwasilisha mchango wake Serikalini. Tuzo hiyo ilikabidhiwa na Mheshimiwa Rais, ikiwa ni ishara ya kutambua mchango wa NIDA katika kuimarisha mapato ya Serikali na kusaidia utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi. 

Akizungumza baada ya hafla hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa NIDA, James Kaji amesema mafanikio hayo ni matokeo ya kuendelea kuimarishwa kwa mifumo ya utoaji huduma kwa wananchi. 

“Tunapokea heshima hii kwa unyenyekevu mkubwa. Mchango huu siyo tu takwimu za kifedha, bali ni matokeo ya uboreshaji wa huduma za utambuzi wa Taifa ambapo ni nyenzo muhimu katika kuimarisha usalama, kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi na kichocheo cha mapato katika sekta binafsi na Umma,” amesema Kaji. 

NIDA inaendelea kutekeleza majukumu yake ya msingi ya kusajili na kuwatambua wananchi kwa kutoa Namba ya Utambulisho wa Taifa (NIN) na Vitambulisho vya Taifa, pamoja na kuwezesha matumizi ya taarifa sahihi za utambuzi katika sekta mbalimbali za huduma za umma na binafsi.

 Utambuzi wa Taifa ni msingi muhimu katika kuwezesha Serikali na Sekta Binafsi kupanga, kuhudumia wananchi au wateja wake kwa ufanisi, kuimarisha usalama, kudhibiti mianya ya udanganyifu na kuongeza tija katika utoaji wa huduma. NIDA inatoa shukrani za dhati kwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa maono, miongozo na uwekezaji unaoendelea kufanywa katika kuimarisha mifumo ya utambuzi nchini.

  Aidha, NIDA inawashukuru wananchi, wadau, taasisi za Serikali na sekta binafsi kwa kuendelea kushirikiana na Mamlaka katika kujenga Taifa lenye utambuzi sahihi, huduma bora na maendeleo jumuishi. Imetolewa na: Kitengo cha Mawasiliano na Hifadhi Hati 




 

Na Victor Masangu, Pwani

Katibu wa siasa,uenezi na Mafunzi wa chama cha mapinduzi (CCM) Dkt. David Mramba amewaasa wananchi hususan vijana kuwa wazalendo na nchi yao na kuachana kabisa na vitendo vya kutumika kwa maslahi ya makundi ya watu wengine na badala yake kuhakikisha wanaweka misingi ya kuwa walinzi na kudumisha amani.

Dkt. Mramba ameyabainisha hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari Ofisini kwake kuhusiana na masuala ya wananchi kuwa na jukumu la kulinda amani katika maeneo yao na kuwahimiza wanapaswa kuzingatia katiba na sheria na kutojiingiza katika vitendo ambayo vinaweza kkuhatarisha usalama wa maisha yao

."Suala la amani ni jambo la muhimu sana katika yetu hivyo niwasihi wananchi wote wa Mkoa wa Pwani msikubali hata kidogo kuwashawishi kufanya vitendo vyovyote ambavyo vinaweza kuhatarisha usalma wa maisha , ikiwemo mali pamoja na uchumi wetu kwani amani ni msingi mkubwa wa maendeleo,"amebainisha Dkt. Mramba .

Aidha Katibu huyo amewahimzia wazazi na walezi kuhakikisha wanawalinda watoto wao na kwamba kila kijana anapaswa kufikiria mustakabali wake ikiwa pamoja na kuweza kulinda amani na kuitunza katika maeneo yao wanayoishi.

Pia Katibu huyo amebainisha kwamba Mkoa wa Pwani umebarikiwa kuwa na lango muhimu la uchumi wa Taifa wakiwemo wakulima,wafugaji ,wavuvi, na wafanyabiashara na wawekezaji kwa hiyo kunahitajika kuwa na mazingira mazuri yenye amani na utulivu.

Mramba pia amewaomba wananchi wote wa Mkoa wa Pwani kuendelea kuwa walinzi wa amani na kwamba wanatakiwa kushirikiana bega kwa bega na vyombo vya dola katika kulinda usalama na tuendelee kujenga Tanzania yenye umoja na mshikamano na maendeleo.

Aidha Katiba amebainisha kwamba chama cha mapinduzi (CCM) Mkoa wa Pwani kinampomgeza na kumuunga mkono Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuwa mstari wa mbela katika kudumisha hali ya amani na utulivu katika Taifa la Tanzania.


Na. Mwandishi Wetu – Dar es Salaam

Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Makatibu Wakuu ya Maandalizi ya Michuano ya Kombe la Mataifa Afrika (AFCON 2027), Dkt. Jim Yonazi, amesema michuano ya AFCON ni fursa adhimu ya kuitangaza Tanzania Kimataifa kupitia sekta mbalimbali ikiwemo ya utalii na uwekezaji hivyo ni jukumu la kila sekta kuhakikisha inachangamkia na kushiriki kikamilifu katika kufanikisha michuano hiyo.

Ameyasema hayo hii leo 01 Julai 2026 wakati wa ziara ya Kamati hiyo inayojumuisha Makatibu Wakuu wa kisekta na baadhi ya wakuu wa Taasisi walipotembelea na kukagua maendeleo ya maandalizi kuelekea michuano hiyo ikiwemo kuangalia miundombinu na vituo vya michezo vitakavyotumika katika michuano ya Kombe la Mataifa Afrika (AFCON 2027) ili kufanikisha mashindano hayo makubwa ya soka barani Afrika.

Katika ziara hiyo, Kamati imekagua maendeleo ya maboresho katika Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Uwanja wa Mazoezi wa Shule ya Sheria (Law School Grounds), Uwanja wa Mazoezi wa Leaders Club, Uwanja wa Mazoezi wa Gymkhana (Gymkhana Club), Uwanja wa Mazoezi wa Farasi pamoja na Uwanja wa Taifa wa Benjamin Mkapa ili kujionea utayari wa miundombinu itakayotumika wakati wa mashindano hayo.

Dkt. Yonazi amesema ili kufanikisha AFCON 2027 kila sekta inapaswa kuweka nguvu ya pamoja katika kuelekea kwenye michuano hiyo kwa kuzingatia faida zake ikiwemo ya kukuza uchumi wa jamii na Nchi kwa ujumla

"AFCON 2027 ni zaidi ya mashindano ya soka; ni jukwaa la kuitangaza Tanzania Duniani hivyo kila taasisi inapaswa kutekeleza wajibu wake ili kuhakikisha nchi inanufaika ipasavyo na fursa hii," amesema Dkt. Yonazi.

Aidha, ameielekeza Bodi ya Utaliii Tanzania (TTB) kuandaa mkakati mahsusi wa kuitangaza Tanzania kupitia mashindano hayo kwa kuonesha vivutio vya utalii, utamaduni na fursa za uwekezaji kwa wageni watakaofika nchini.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Maendeelo ya Michezo kutoka Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Bw. Boniface Tamba, amesema maboresho ya miundombinu yanaendelea vizuri na kwamba ujenzi wa barabara zinazoingia na kutoka katika vituo pamoja na viwanja vya michezo umefikia hatua za mwisho za ukamilishaji.

"Maandalizi yanaendelea kwa kasi na miundombinu muhimu ipo katika hatua za mwisho ili kuhakikisha Tanzania inakuwa tayari kuandaa AFCON 2027 kwa viwango vinavyotakiwa," amesema Bw. Tamba.

Kamati ya Makatibu Wakuu inaendelea na ziara ya ukaguzi wa miundombinu ya AFCON 2027, ambapo baada ya kukamilisha ukaguzi katika Mkoa wa Dar es Salaam itatembelea Zanzibar kabla ya kuhitimisha ziara hiyo itatembelea katika viwanja vilivyopo Jijini Arusha.















Top News