-Naibu Waziri Kwagilwa aahidi kufanya ziara katika halmashauri 184 kukagua zoezi hilo


Na Ashura Mohamed - ARUSHA

Serikali imesema haitamuonea haya mtu yeyote atakayefanya maigizo katika zoezi la upandaji miti nchini, ikieleza kuwa zoezi hilo ni muhimu kwa mustakabali wa mazingira.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, Mhe. Reuben Nhamanilo Kwagilwa, wakati wa uzinduzi wa Kituo cha Jamii cha Ustahimilivu wa Mabadiliko ya Tabianchi - CCRC, kilichopo Chuo cha Maendeleo ya Jamii Tengeru - TICD.

Mhe. Kwagilwa amesema baada ya kumalizika kwa Bunge la Bajeti ataomba idhini kwa Waziri wa Mazingira kufanya ziara ya kukagua utekelezaji wa upandaji miti katika halmashauri zote 184 nchini ili kujionea hali halisi.

“Bunge hili likiisha nitataka kama serikali kwenda kuangalia hali halisi ya upandaji miti. Kwa kuwa kila mkurugenzi anayeulizwa anasema tumepanda miti milioni 5, milioni 2, lakini ukikagua eneo hilo miti hutaiona kabisa. Maigizo haya ndugu zangu kwenye mazingira ni hatari,” alisema.

Aliongeza kuwa serikali itamchukulia hatua mtu yeyote atakayethibitika kuendeleza shughuli za uharibifu wa mazingira baada ya kupewa taarifa.

Naibu Waziri ameeleza kuwa chanzo kikubwa cha mabadiliko ya tabia nchi ni uharibifu wa vyanzo vya maji, ukataji miti, kilimo kisichozingatia uhifadhi wa ardhi, pamoja na shughuli za viwanda, uvuvi na uchimbaji wa madini usiozingatia utaratibu.

Hali hiyo imesababisha ukame usioelezeka, mvua zisizo na majira, mafuriko, mito kubadilisha mikondo, maziwa kuingia kwenye makazi ya watu, dhoruba na vimbunga.

“Chanzo kikubwa cha uharibifu wa mazingira ni  uchafuzi wa vyanzo vya maji, ukataji misitu, kilimo ambacho hakiipi ardhi yetu ikolojia,hali inayochangia ongezeko la  gesi joto kwenye ikolojia ya uso wa dunia na kupelekea mabadiliko ya tabia nchi ambayo tunayaona leo,” alisema Kwagilwa.

Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo cha Maendeleo ya Jamii TICD, Dkt. Bakari George amesema kituo hicho kitashirikiana na jamii na wadau mbalimbali kuandaa sera na kufanya tafiti za kusaidia jamii kuondokana na janga la mabadiliko ya tabia nchi.

Meneja wa CCRC, Dkt. Agnes Kapinga amesema uanzishwaji wa kituo hicho umefuata uchafuzi mkubwa wa mazingira unaopelekea ongezeko la taka kila siku na mifumo kushindwa kustahimili.

“Uwepo wa kituo hicho kwa kushirikiana na taasisi zingine utakujia na majibu ya changamoto mbalimbali zitakazosaidia jamii na taifa kwa ujumla kuwa na ustahimilivu kwa maendeleo endelevu,” alisema Dkt. Kapinga.

Kwa mujibu wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM inamtaka kila Mkurugenzi wa Halmashauri nchini kuhakikisha anapanda miti milioni 1.5 ili kukabiliana na uharibifu wa mazingira na mabadiliko ya tabia nchi.

Naibu waziri wa nchi Ofisi ya Mkuu wa Raisi Muungano na Mazingira Mh.Reuben Nhamanilo Kwagila akizungumza katika hafla hiyo
Naibu waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira akikata Utepe wakati wa Uzinduzi wa kituo Cha Jamii Cha Ustahimilivu wa Mabadiliko ya Tabianchi
Mkuu wa chuo Cha Maendeleo ya Jamii Tengeru (TICD),Dkt.Bakari George akizungumza wakati wa hafla hiyo iliyofanyika chuoni hapo




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi, wananchi pamoja na Maafisa mbalimbali wa Jeshi la Polisi kabla ya kuhitimisha Mafunzo ya Maafisa na Wakaguzi Wasaidizi wa Jeshi la Polisi, kozi namba 1 ya mwaka 2025/2026 katika Chuo cha Taaluma ya Polisi, Kurasini Jijini Dar es Salaam, tarehe 28 Mei, 2026.
Viongozi mbalimbali wakiwa kwenye hafla ya kuhitimisha Mafunzo ya Maafisa na Wakaguzi Wasaidizi wa Jeshi la Polisi, kozi namba 1 ya mwaka 2025/2026 katika Chuo cha Taaluma ya Polisi, Kurasini Jijini Dar es Salaam, tarehe 28 Mei, 2026.
Wahitimu wa kozi namba 1 ya mwaka 2025/2026 kwa Maafisa na Wakaguzi Wasaidizi wa Jeshi la Polisi Tanzania wakiwa kwenye hafla ya kuhitimu Mafunzo hayo katika Chuo cha Taaluma ya Polisi, Kurasini Jijini Dar es Salaam, tarehe 28 Mei, 2026.

Kikundi cha Kibati kikitumbuiza kwenye hafla ya kuhitimisha Mafunzo ya Maafisa na Wakaguzi Wasaidizi wa Jeshi la Polisi, kozi namba 1 ya mwaka 2025/2026 katika Chuo cha Taaluma ya Polisi, Kurasini Jijini Dar es Salaam, tarehe 28 Mei, 2026.


















Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amewasili Chato Mkoani Geita, ambapo anatarajiwa kumwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Mazishi ya Marehemu Bi. Suzana Magufuli ambaye ni Mama wa aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, yatakayofanyika tarehe 29 Mei 2026 Wilayani Chato.

Makamu wa Rais amepokelewa katika Uwanja wa Ndege Geita, Wilayani Chato, Mapokezi yaliyoongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhe. Martin Shigela, Viongozi wa Kamati ya Ulinzi na Usalama, Viongozi wa Chama Cha Mapinduzi pamoja na Viongozi mbalimbali Waandamizi.

Pia Makamu wa Rais, amefika nyumbani kwa marehemu,Bi Suzana Magufuli, Kilimani Chato, kwa lengo la kusaini kitabu cha maombolezo pamoja na kuwafariji wafiwa kufuatia msiba huo.












Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni, Songoro Mnyonge, amemwelekeza Mkurugenzi wa Manispaa hiyo, Hanifa Suleiman Hamza, kuchukua hatua kali za kuwaondoa mara moja watu wanaofanya biashara kiholela katika eneo la Daraja la Tanzanite, hususan jirani na makazi ya mabalozi jijini Dar es Salaam.

Aidha, amemwelekeza mkurugenzi huyo kupitia Idara ya Ustawi wa Jamii kuwaondoa ombaomba wote katika makutano ya Barabara ya Kinondoni na Ali Hassan Mwinyi, akieleza kuwa shughuli wanazofanya katika eneo hilo kwa kiasi kikubwa zinatweza utu wa binadamu.

Meya Mnyonge alitoa maelekezo hayo leo Mei 28, 2026, katika kikao cha Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni.

OPERESHENI OMBAOMBA

“Mkurugenzi, wimbi la ombaomba limeendelea kuongezeka Kinondoni. Baadhi ya maeneo yamekuwa kero kubwa kwa ombaomba, wengine ni watoto waliotakiwa kwenda shule, Eneo la Barabara ya Kinondoni karibu na Ubalozi wa Urusi na Benki ya Stanbic mkafanye mkakati waondolewe pale,” amesema Meya Mnyonge.

Ameeleza kuwa katika eneo hilo watu wanaojihusisha na ombaomba wamekuwa wakipika, kufua na kulala, huku baadhi yao wakiwa ni watoto wadogo.

“Watoto wanagonga vioo vya magari kuomba na wengine wanafuta vioo, hali inayohatarisha hata usalama wao. Ofisa Ustawi wa Jamii wa Manispaa afanye mkakati waondolewe.”

Kuhusu ongezeko la wafanyabiashara katika eneo la Daraja la Kisasa la Tanzanite, hasa upande wa makazi ya mabalozi, Meya Mnyonge amesema eneo hilo limegeuzwa soko kinyume cha utaratibu.

“Daraja la Tanzanite katika nyumba za mabalozi pamegeuzwa soko. Pale kuna mabalozi. Eneo hilo wameligeuza soko la kufanya biashara mpaka usiku, Watu wanaokesha pale wanajisaidia wapi? Hii ina maana wao ndiyo wanahusika na uchafuzi wa mazingira, Inatweza utu wa binadamu Lile eneo siyo soko waondolewe.”

Amebainisha kuwa ongezeko la watu wasioeleweka katika maeneo hayo linawatia hofu mabalozi, kwani huenda hata watu wenye nia ovu wakajichomeka miongoni mwa wafanyabiashara hao.

Katika hatua nyingine, Meya Songoro ameipongeza Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni kupitia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) kwa kuanza operesheni ya kuondoa magari mabovu yaliyokuwa yameegeshwa katika maeneo ya watembea kwa miguu kwenye Barabara ya Tandale.

“Magari yameondolewa, sasa Tandale unaweza kupita pande zote za barabara. Tunachofanya sasa ni kuwatafutia eneo maalumu watu waliokuwa wanafanya biashara ya kuuza magari hayo mabovu, Hatuwezi kuwaondoa kwa sababu bado hatujapata eneo la kuwapeleka. Kilichofanyika ni magari hayo kuondolewa katika eneo la barabara na kusogezwa katika makazi yao.”

MARUFUKU GURIO BIAFRA

Meya Mnyonge pia amemwelekeza Mkurugenzi Hanifa kufunga shughuli zote za biashara zisizo rasmi katika eneo la viwanja vya Biafra.

“Biafra imegeuzwa gurio. Hakuna gurio pale. Unafika wakati wanafunga mpaka barabara. Kama kuna mtu ameweka gurio pale, liondolewe. Lilianza kidogo sasa limefika mpaka Msikiti wa Mtambambani.”

RASIMU YA SHERIA NDOGO YAPITISHWA

Katika hatua nyingine, Baraza la Madiwani la Manispaa ya Kinondoni limepitisha Rasimu ya Sheria Ndogo za Manispaa hiyo ya mwaka 2026.

“Tumepitisha Rasimu ya Sheria Ndogo ya Manispaa ya Kinondoni inayozingatia Sura ya 288 ya mwaka 2023. Rasimu hii inahusisha vyanzo mbalimbali vya mapat”.

Amesema sheria hizo ndogo ni pamoja na Sheria ya Ada na Ushuru ya Manispaa ya Kinondoni ya mwaka 2026, ambayo pia inawataka watu wenye mabwawa ya kuogelea ya kibiashara kulipia ushuru wa shilingi 100,000 kwa mwaka.

Ameeleza kuwa rasimu hiyo itaanza kutumika mara baada ya kupitishwa na Waziri wa Fedha, Dk. Mwigulu Nchemba, kuwa sheria rasmi.











Na Mwandishi Wetu, Siha

Wilaya ya Siha mkoani Kilimanjaro inatarajiwa kupokea zaidi ya washiriki 800 kutoka ndani na nje ya Tanzania katika mashindano makubwa ya michezo na utalii yajulikanayo kama West Kili Forest Tour Challenge, yatakayofanyika Juni 20 hadi 21, 2026 katika ukanda wa msitu wa West Kilimanjaro.

Mashindano hayo yamezinduliwa rasmi na Mkuu wa Wilaya ya Siha, Dkt. Christopher Timbuka, aliyesema tukio hilo litakuwa chachu ya kuitangaza Siha kimataifa kupitia utalii wa asili, michezo na shughuli za kijamii zitakazochochea uchumi wa wananchi.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Dkt. Timbuka alisema mashindano hayo yatahusisha mbio za kilomita 5, 10 na 21, pamoja na mashindano ya baiskeli na pikipiki yatakayopita katika maeneo yenye mandhari ya kuvutia ya msitu wa West Kilimanjaro.

“Tunatarajia kupokea washiriki wengi kutoka sehemu mbalimbali za Tanzania na nje ya nchi. Hii ni fursa kubwa kwa Siha kuendelea kujitangaza kama kitovu cha utalii wa michezo na uhifadhi wa mazingira,” alisema Dkt. Timbuka.

Aliongeza kuwa maandalizi yote muhimu yamekamilika ili kuhakikisha mashindano hayo yanafanyika kwa mafanikio makubwa huku yakitoa nafasi kwa wananchi kunufaika kupitia biashara mbalimbali zikiwemo malazi, chakula, usafiri na huduma nyingine za kijamii.

Kwa mujibu wa waandalizi, kabla ya siku ya mashindano kutafanyika mkesha maalumu wa burudani utakaojumuisha shughuli za kijamii, muziki, chakula na vinywaji kwa washiriki na wadau mbalimbali.

Mashindano hayo yanaungwa mkono na kampuni ya Mati Super Brands Ltd ambayo imeahidi kushirikiana kuhakikisha tukio hilo linakuwa la kipekee na lenye mafanikio makubwa.

Akizungumza kuhusu malengo ya mashindano hayo, Mratibu wa West Kili Forest Tour Challenge, Bw. Mensier Elly, alisema tukio hilo si la michezo pekee bali ni jukwaa muhimu la kutangaza vivutio vya utalii vya West Kilimanjaro na kuhamasisha uhifadhi wa mazingira kupitia michezo na utalii endelevu.

“Tunataka kutumia michezo kama njia ya kuhamasisha jamii kuthamini mazingira na wakati huo huo kuitangaza West Kilimanjaro kwa dunia,” alisema Bw. Elly.

Mashindano hayo yanatarajiwa kuwa miongoni mwa matukio makubwa ya michezo na utalii nchini mwaka huu kutokana na ushiriki mkubwa unaotarajiwa pamoja na mvuto wa kipekee wa mazingira ya West Kilimanjaro.





















Top News