Na Janeth Raphael- MichuziTv -Dodoma 

Katibu wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Kenani Kihongosi, amesema kuwa changamoto ya kupanda kwa bei ya mafuta ni ya kidunia na si ya Tanzania pekee, hivyo haipaswi kuingizwa katika mjadala wa kisiasa.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Aprili 7, 2026, katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi Kuu ya CCM jijini Dodoma, Kihongosi alisema nchi nyingi duniani, zikiwemo zile zenye uchumi mkubwa, zimeathirika na hali hiyo na zimepitia wakati mgumu kutokana na kupanda kwa bei za mafuta.

Alisisitiza kuwa katika kukabiliana na changamoto hiyo, ni muhimu kuwepo kwa ukweli na mshikamano wa kitaifa badala ya kubeba masuala ya kisiasa yanayoweza kupotosha wananchi.

Aidha, Kihongosi alimkosoa mmoja wa viongozi wa kisiasa kwa kutoa kauli kuhusu suala hilo bila kuwa na uelewa wa kutosha wa masuala ya uchumi. Alimtaka kujielimisha zaidi kabla ya kuzungumzia mambo nyeti yanayohusu maisha ya wananchi.

Katika hatua nyingine, alimzungumzia John Heche, akimtaka kutumia zaidi viongozi wenye uelewa wa masuala ya uchumi ndani ya chama chake, akiwemo Katibu Mwenezi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), ili kuepuka upotoshaji wa taarifa kwa umma.

Kihongosi aliongeza kuwa Watanzania wanafahamu kuwa kupanda kwa bei ya mafuta ni changamoto ya kimataifa, na akasisitiza umuhimu wa nchi kuungana katika kutafuta suluhisho, kama ilivyofanyika wakati wa janga la COVID-19.

Alimalizia kwa kutoa wito wa kudumisha umoja, mshikamano na upendo miongoni mwa wananchi ili kuweza kukabiliana kwa pamoja na changamoto zinazolikabili taifa kwa sasa.

Kwa sasa, wataalamu wa uchumi wanaeleza kuwa kupanda kwa bei ya mafuta kunachangiwa na mambo mbalimbali ikiwemo mabadiliko ya soko la kimataifa, migogoro ya kisiasa katika baadhi ya maeneo yanayozalisha mafuta, pamoja na ongezeko la mahitaji ya nishati duniani.

 Hali hii imeendelea kuathiri gharama za maisha kwa wananchi katika nchi nyingi, ikiwemo Tanzania, hivyo kuhitaji mikakati madhubuti ya muda mfupi na mrefu ili kupunguza athari zake kwa uchumi wa taifa.




Na Munir Shemweta, Nairobi

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt Leonard Akwilapo, anatarajiwa kuongoza ujumbe wa Tanzania kushiriki Kongamano la Pili la Jukwaa la Miji Afrika (2nd African Urban Forum) litakalofanyika kuanzia tarehe 8 hadi 10 Aprili 2026 katika jiji la Nairobi nchini Kenya.

Kongamano hilo linaongozwa na kauli mbiu isemayo “Adequate Housing for All: Advancing Socio-Economic and Environmental Transformation Towards the Realization of Agenda 2063,” linalenga kuhamasisha mijadala itakayotoa fursa kwa washiriki kutoka nchi mbalimbali za Afrika kubadilishana uzoefu na suluhisho bunifu katika kukabiliana na changamoto za maendeleo ya miji na makazi.

Kupitia kongamano hilo, Tanzania inatarajiwa kutoa tamko la nchi litakaloeleza jitihada za Serikali katika kuchochea maendeleo endelevu ya miji na makazi, ikiwa ni pamoja na sera, mipango na mikakati inayotekelezwa kuboresha makazi na upangaji wa miji.

Aidha, Mhe. Dkt Akwilapo atashiriki katika mijadala ya ngazi ya juu itakayowahusisha mawaziri, mameya na wataalamu mbalimbali, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kimataifa katika sekta ya maendeleo ya miji.

Awali Dkt Akwilapo aliongoza kikao cha maandalizi kwa ujumbe wa Tanzania utakaoshiriki kongamano hilo katika ubalozi wa Tanzania nchini Kenya tarehe 7 April, 2026 ambapo masuala mbalimbali ya uwakilishi wa nchi yalijadiliwa.

Dkt Akwilapo ameambatana na Mkurugenzi wa Maendeleo ya Makazi Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Bw. Deogratias Kalimenze, Mkurugenzi Msaidizi Uzingatiaji Mipango ya Matumizi ya Ardhi kutoka Tume ya Taifa ya Matumizi ya Ardhi Bi. Rehema Kishoa, Maafisa kutoka Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi pamoja na taasisi binafsi.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (Kushoto) akimsikiliza kwa makini Balozi wa Tanzania nchini Kenya Mhe. Dkt Bernard Yohana Kibesse (Kulia) kabla ya kuanza kikao cha maandalizi ya ushiriki wa Tanzania katika Kongamano la Miji Afrika litakalofanyika jijini Nairobi kuanzia tarehe 8 hadi 10 April 2026.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akisaini kitabu cha wageni katika ofisi za ubalozi wa Tanzania Nchini Kenya mara baada ya kuwasili ubalozini katika kikao cha maandalizi ya ushiriki wa Tanzania katika Kongamano la Miji Afrika litakalofanyika jijini Nairobi kuanzia tarehe 8 hadi 10 April 2026.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akioongoza kikao cha maandalizi ya ushiriki wa Tanzania katika Kongamano la Miji Afrika kwa ujumbe wa Tanzania katika ubalozi wa Tanzania jijini Nairobi tarehe 7 April 2026.

Balozi wa Tanzania nchini Kenya Mhe. Balozi Dkt Bernard Yohana Kibesse akizungumza katika kikao cha maandalizi ya ushiriki wa Tanzania katika Kongamano la Miji Afrika litakalofanyika jijini Nairobi kuanzia tarehe 8 hadi 10 April 2026. Kushoto ni Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo na Kulia ni Mkurugenzi wa Maendeleo ya Makazi Wizara ya Ardhi Bw, Deogratias Kalimenze.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akisaini kitabu cha wageni katika ubalozi wa Tanzania nchini Kenya. Kulia ni Balozi wa Tanzania nchini Kenya Mhe Balozi Dkt Bernard Yohana Kibesse na Katikati ni Mkuu wa Utawala katika Ubalozi wa Tanzania nchini Kenya Bi Eliet Magogo (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI).



BANK of Africa Tanzania imeendelea kutekeleza sera yake ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) kwa kutoa kiasi cha shilingi milioni 24 kwa vituo vinne vinavyolea watoto wanaoishi katika mazingira magumu, ikiwa ni juhudi za kuboresha maisha yao hususan katika mahitaji ya chakula na elimu hapa nchini.

Mkuu wa Kitengo cha Masoko na Mawasiliano wa benki hiyo, Nandi Mwiyombella, alisema vituo vilivyonufaika na msaada huo ni Amani Foundation for Orphanage Centre (Zanzibar), UMRA Orphanage Centre (Dar es Salaam), Kijiji cha Furaha (Dar es Salaam) na Kalamu Education Foundation (Dar es Salaam).

Alisema kiasi hicho cha fedha kimegawanywa sawa, ambapo kila kituo kitapata shilingi milioni 6 kwa ajili ya chakula na vifaa vya shule ili kusaidia watoto hao kuendelea na masomo yao.

“Hiki kiasi si kikubwa wala kidogo, bali ni sehemu ya sera ya kusaidia jamii. Tunataka kuhakikisha watoto wanaoishi katika mazingira magumu wanapata mahitaji muhimu ya msingi,” alisema Mwiyombella.

Aliongeza kuwa benki hiyo inatoa wito kwa taasisi nyingine za kifedha nchini kuona umuhimu wa kusaidia makundi maalum katika jamii kama njia ya kupunguza umasikini na kuwawezesha watoto ambao ni taifa la kesho.

“Dhamira yetu kama benki ni kuthamini ukuaji wa pamoja na utu wa mwanadamu. Kwa kutoa msaada huu, tunalenga kuunga mkono juhudi za vituo hivi katika kuwalea na kuwaendeleza watoto hawa,” alisisitiza.

Aidha, alifafanua kuwa kabla ya kutoa msaada wowote, benki hushirikiana na jamii husika, ikiwemo halmashauri na uongozi wa vituo, ili kubaini mahitaji halisi yanayohitaji kipaumbele.

Kwa upande wake, Meneja Mradi wa Kalamu Education Foundation (KEF), Dkt. Saidy Ally Soudy, aliishukuru benki hiyo kwa msaada wa fedha na chakula, akisema utasaidia kwa kiasi kikubwa kuboresha ustawi wa watoto wanaolelewa katika kituo hicho.

“Kituo chetu kinawasaidia watoto wanaoishi katika mazingira magumu na kina dhamira ya kuwasaidia kufikia ndoto zao kielimu. Msaada huu wa vifaa na chakula ni muhimu sana,” alisema Dkt. Soudy.

Naye Msimamizi wa Kijiji cha Furaha, Martha Massawe, alisema lengo la kituo hicho ni kuwasaidia watoto kupata elimu ya msingi na sekondari, huku akitoa shukrani kwa msaada huo uliosaidia pia ujenzi na upanuzi wa kituo hicho kilichoanzishwa mwaka 2002 katika eneo la Mbweni, Dar es Salaam.

Kwa upande wake, Katibu wa UMRA Orphanage Centre, Hamza Ahmed, alisema msaada huo ni muhimu katika kuwasaidia watoto kujiandaa kwa maisha ya baadaye na kujitegemea.

“Tunawapongeza Bank of Africa Tanzania kwa msaada huu adhimu. Ni mchango mkubwa katika kuboresha maisha ya watoto wetu,” alisema Ahmed.

Akizungumza kwa niaba ya watoto wenzake, Zuwena Abbas Ali kutoka Amani Foundation alitoa shukrani kwa benki hiyo kwa msaada walioupata, akisema unawasaidia katika maisha yao ya kila siku na masomo.

Mpango huo unaashiria dhamira ya kudumu ya Bank of Africa Tanzania katika uwajibikaji kwa jamii, huku ukilenga kuboresha maisha ya watoto wanaoishi katika mazingira magumu katika maeneo ya Zanzibar na Dar es Salaam.

Ikizingatiwa kuwa vituo vya malezi hukumbwa na changamoto za mara kwa mara katika upatikanaji wa chakula na mahitaji ya msingi, benki hiyo ilitoa msaada huo ili kusaidia uendeshaji wa vituo hivyo na kuhakikisha huduma muhimu zinapatikana kwa watoto.
Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa Bank of AfricaTanzania, Nandi Mwiyombella (kulia), alikabidhi nyaraka za mradi kwa Sister Martha Massawe, Msimamizi wa Kijiji cha Furaha kilichopo Mbweni, Dar es Salaam. Makabidhiano hayo yamefuatia mchango wa kifedha uliotolewa na Benki kusaidia ununuzi wa vifaa vya ujenzi kwa ajili ya ujenzi wa ofisi mpya ya kituo hicho. 
Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa Benki hiyo, Nandi Mwiyombella (katikati) akipeana mkono na Meneja wa Kalamu Education Foundation (KEF),Dkt. Saidy Ally Soudy, baada ya kukabidhi msaada wa vyakula.
Meneja Masoko na Mawasiliano wa Bank of Africa Tanzania, Nandi Mwiyombella (kulia), akitoa msaada wa mtungi wa gesi na vyakula kwa Katibu wa Kituo cha Yatima cha Umrah, Hamza Ahmed (kushoto), katika hafla ya kuimalisha ushirikiano na jamii, Dar es Salaam juzi.
Wafanyakazi wa Bank of Africa Tanzania wakiwa katika picha ya pamoja viongozi wa Taasisi ya KEF.

Vijana wakiwezeshwa kuendesha miradi mbalimbali ikiwemo ya kilimo wataweza kujikwamua kiuchumi kama wanavyoonekana vijana wakiwa shambani kwenye mradi wa kilimo cha mboga wa Matongo unaofadhiliwa na Barrick North Mara (Picha kutoka maktaba)

Mgodi wa Barrick North Mara uliopo wilayani Tarime katika mkoa wa Mara umeendelea kutekeleza moja ya sera ya mkakati endelevu wa kampuni ya kuwezesha wananchi wanaoishi jirani na migodi yake kuwa na maisha bora ambapo kupitia fedha za uwajibikaji kwa jamii (CSR) umetoa shilingi milioni 220 kwa vikundi 13 vya vijana ili kuanzisha miradi ya kiuchumi katika vijiji vyote 11 vinavyozunguka mgodi huo.


Hatua hii ni mwendelezo wa mgodi wa Barrick North Mara kuwezesha kiuchumi makundi mbalimbali katika jamii hususani vijana ambapo mwaka jana iliunga mkono jitihada za Serikali za kuwapatia leseni za uchimbaji ambapo mgodi ulitoa leseni zake na kufadhili mafunzo ya vijana hao zaidi ya 1700 wanaojiandaa kuingia katika uchimbaji wa madini chini ya programu ya Mining For a Brighter Tomorrow (MBT) inayolenga kuboresha usalama, kuongeza tija na kuondoa uvamizi wa mgodi kwa kuwapatia rasmi maeneo ya uchimbaji.


Tayari vikundi hivyo vimepokea fedha hizo, ikiwa ni ruzuku ya (CSR) ya mwaka uliopita kutoka kwa mgodi huo ambao unaendeshwa kwa ubia na serikali kupitia kampuni ya Twiga Minerals.


Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jami wa Halmashauri hiyo, Anthony George Nyange amesema kuwa fedha hizo zimesaidia vijana takriban 100 wanachama wa vikundi hiyo kuanzisha miradi ya mbalimbali ya kiuchumi.

Anthony George Nyange


“Nawashukuru sana Barrick North Mara hususan idara ya mahusiano ya jamii kwa ushirikiano ambao wamekuwa wakitoa katika kufanikisha mpango huu wa ruzuku ya uwajibikaji kwa jamii kwa vijana,” amesema Nyange.


Nyange amesema miradi hiyo imesaidia kutatua changamoto mbalimbali zilizokuwa katika vijiji hivyo kwa ajili ya ustawi wa jamii vinavyouzunguka mgodi huo.


“Wanufaika wengi ni vijana na wamejielekeza kwenye miradi ambayo siyo tu kwa ajili ya kujipatia kipato bali pia kutatua changamoto zilizokuwepo,” amesema.


Ametaja vikundi ambavyo vimenufaika na mpango huo kuwa ni Mokarambe Agribusiness, Hope and Revolution of Economy for Youth, Tunza Mazingira Nyamongo, Amshana Nyamongo na REMHOCHI.


Vingine ni Kazi ni Moyo, Konna Nne, Kiumanya, Ibuka Umoja, Tunaweza Kerende, Nyasa Group, Mtazamo Youth na Kikundi cha Keryoba.


Amesema baadhi ya vikundi hivyo vimeanzisha miradi ya usafi wa mazingira jambo ambalo limesaidia kuweka mji mdogo wa Nyamongo katika hali nzuri ya usafi na mazingira.


“Kwa mfano, kulikuwa na changomoto ya usafi katika mji wa Nyamongo, sasa hali ya usafi ni nzuri kwa sababu kuna kikundi cha mazingira ambacho kinafanya vizuri sana kwenye usafi wa mazingira,” amesema Nyange.


Nyange amesema Halmashauri ya Wilaya ya Tarime itaendelea kutenga sehemu ya fedha za Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) zinazotolewa na mgodi wa Barrick North Mara kwa ajili ya kuwawezesha vijana kuanzisha na kuendeleza miradi ya kiuchumi.


“Tunategemea na mwaka huu pia tutatenga sehemu ya CSR kwenda kuwezesha vijana kwenye miradi ya kiuchumi. Sasa hivi, vijana wengi kule Nyamongo wana shughuli za kufanya kujipatia kipato na hata vitendo vya kihalifu vimepungua,” amesema Nyange.


Amesema mbali na mpango wa Uwajibikaji kwa Jamii (CSR), vijana hao pia wamenufaika na mikopo kupitia asilimia 10 ya mapato ya ndani inayotolewa na halmshauri hiyo kuwezesha wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.


“Wanufaika wakubwa ni vijana, na mbali ya kunufaika na mikopo yetu ya halmashauri ya asilimia 10, pia wamenufaika na mpango wa ruzuku ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) kwa vijana,” amefafanua Nyange.


Taarifa zinaonesha Halmashauri ya Wilaya ya Tarime inaongoza kwa kutoa kiasi kikubwa cha mikopo ya asilimia 10 kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu katika Mkoa wa Mara.


Mgodi wa Barrick North Mara pamoja na kutekeleza sera ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) pia utoaji wa leseni za uchimbaji kwa vijana uliwezesha na mafunzo ya siku 14 yaliyofanywa kwa kushirikiana na serikali.


Lengo la mafunzo hayo ni kuhakikisha sekta ya madini inakuwa na tija zaidi kwa kuzingatia usalama mahali pa kazi na utunzaji wa mazingira , usimamizi wa biashara za madini na kufuata sheria za nchini na usimamizi wa vikundi pamoja na elimu ya masuala ya fedha.

Mkuu wa wilaya ya Ilala, Mheshimiwa Edward Mpogolo, ambaye amemuwakilisha Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam Mheshimiwa Albert Chalamila, amepongeza na kuwashukuru viongozi wa dini kwa mchango wao mkubwa wa kuimarisha na kudumisha amani lengo kuleta maendeleo katika jamii.

Akizungumza katika maadhimisho ya kumbukumbu ya miaka 19 ya kanisa la WRC Kivule tarehe,6 April, DC Mpogolo alisema licha ya changamoto mbalimbali viongozi wa dini wameendelea kujitoa na kushirikiana na serikali pale wanapohitajika.

Aidha alimpongeza mgeni rasmi, Deus Sangu, Waziri wa nchi ofisi ya waziri mkuu kazi na ajira , ambaye alimuwakilisha makamu wa raisi Mheshimiwa Emmanuel Nchimbi kwa kushiriki katika maadhimisho hayo.

DC Mpongolo ameipongeza serikali chini ya Mheshimiwa raisi Dkt Samia Suluhu Hassan kwa juhudi zake za kuleta maendeleo kwa utoaji wa fedha katika mkoa huo na kusisitiza kuwa mafanikio hayo yasingewezekana bila uwepo wa amani, maadili na mchango wa viongozi wa dini.

Aliongeza kuwa viongozi wa dini wamekuwa nguzo muhimu katika kuleta amani, utulivu, upendo na mshikamano miongoni mwa wananchi na kujenga jamii kupitia hofu ya Mungu hali inayochangia kwa kiasi kikubwa utekelezaji wa malengo ya serikali.

“Mgeni rasmi kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam tufikishie salamu kwa raisi wetu amekuwa na mafanikio makubwa lakini mafanikio haya ni kutokana na maombi ya viongozi wetu na waumini”

Mheshimiwa Mpogolo aliwataka waumini na wananchi kwa ujumla kuendelea kumuombea Rais pamoja na kudumisha amani, akibainisha kuwa mafanikio ya Taifa yanatokana na ushirikiano wa viongozi wa dini na wananchi kwa ujumla.















 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akishiriki Dua maalum ya kumuombea aliyekuwa Rais wa kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Hayati Abeid Amani Karume ikiwa ni miaka 54 tangu kuuawa kwake.

Dua hiyo maalum imefanyika Afisi Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kisiwandui, Zanzibar tarehe 7 Aprili, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akishiriki Dua maalum mbele ya kaburi la aliyekuwa Rais wa kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Hayati Abeid Amani Karume ikiwa ni miaka 54 tangu kuuawa kwake, Afisi Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kisiwandui, Zanzibar tarehe 7 Aprili, 2026.

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan akiweka Shada la Maua katika Kaburi la Rais wa Kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Hayati Abeid Amani Karume mara baada ya Dua iliyofanyika katika Afisi Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM) Kisiwandui Zanzibar leo tarehe 07 Aprili 2026, katika Siku ya Kumbukumbu ya (Karume Day).

 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan akiwa pamoja na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mheshimiwa Dkt. Hussein Ali Mwinyi wakati wa kuweka Shada la Maua katika Kaburi la Rais wa Kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Hayati Abeid Amani Karume mara baada ya Dua iliyofanyika katika Afisi Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM) Kisiwandui Zanzibar leo tarehe 07 Aprili 2026, katika Siku ya Kumbukumbu ya (Karume Day).













 

Na Mwandishi Wetu.

*DODOMA* : MAMLAKA ya Uteuzi imeridhia maombi ya muda wa ziada kwa Tume ya Kuchunguza Matukio ya Uvunjifu wa Amani Wakati na Baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025 hivyo imeiongezea tena muda wa siku ishirini na moja (21) na kuitaka ikamilishe kazi kabla au ifikapo Aprili 24, 2026.

Mamlaka hiyo imeeleza sababu za kuongeza muda huo kwa Tume ni pamoja na kuiwezesha Tume kukamilisha uchambuzi wa ushahidi, taarifa na maoni yaliyopokelewa, kutoa fursa kwa wataalamu wa uchunguzi wa kisayansi kufanyia kazi baadhi ya vielelezo vipya vilivyowasilishwa.

Sababu nyingine ni kuiwezesha Tume kukamilisha maandalizi ya Ripoti itakayowasilishwa kwa Rais na kutoa fursa kwa Tume kuandaa tafsiri ya Ripoti hiyo.

Tume hiyo ilianza kutekeleza majukumu yake Novemba 20, 2025 na kutarajiwa kukamilisha kazi yake ndani ya kipindi cha siku 90. Hata hivyo, kutokana na sababu mbalimbali, Tume iliongezewa muda wa kukamilisha kazi na kutakiwa kuwasilisha Ripoti kwa Rais kabla au ifikapo April 3, 2026.

Hivyo, kufuatia nyongeza ya muda, wananchi waliendelea kujitokeza kwa wingi tofauti na matarajio ya Tume. Hivyo, Tume iliendelea kupokea ushahidi, taarifa na maoni zaidi. 

Kwa sababu hiyo, Tume haikuweza kukamilisha kazi yake ndani ya muda wa nyongeza uliotolewa na hivyo kulazimika kuomba muda wa ziada ili kukamilisha kazi yake. 

Tume inaendelea kuwashukuru wananchi na wadau wote waliotoa ushirikiano kwa Tume wakati wa kufanya uchunguzi, ikiwemo wale waliofika mbele ya Tume kutoa ushahidi, taarifa na maoni, waliopiga simu na kutuma ujumbe, waliotuma ushahidi, taarifa na maoni kwa maandishi na waliowasiliana na Tume kwa njia za mitandao ya kijamii.


 


-Asema Serikali itatoa kauli baada ya uchunguzi

-Aagiza vibanda vipya vigawiwe kwa wafanyabiashara halisi


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, ameagiza hatua za haraka kurejesha shughuli za biashara kufuatia ajali ya moto ulioteketeza Soko la Mawasiliano (Simu 2000) lililopo katika Kata ya Sinza, Wilaya ya Ubungo jijini Dar es Salaam.

Ameyasema hayo Aprili 6, 2026, alipofika kukagua madhara ya tukio hilo la moto lililotokea Aprili 4, 2026, ambapo takribani vibanda 500 vya wafanyabiashara wadogo viliteketea.

Akizungumza na wafanyabiashara hao, Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea kufuatilia kwa karibu tukio hilo na itatoa kauli rasmi baada ya kukamilika kwa uchunguzi wa kina ulioelekezwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.

“Mheshimiwa Rais amepata taarifa ya jambo hili, anawapa pole sana na ameelekeza uchunguzi wa kina ufanyike ili tujue chanzo cha tatizo hili. Na kazi hiyo imekwisha kuanza ili tuweze kupata undani wa chanzo cha jambo hili lililojitokeza,” amesema.

Aidha, Waziri Mkuu ameagiza eneo la soko hilo kusafishwa mara moja ili kuruhusu wafanyabiashara kuanza taratibu za kurejesha shughuli zao.

“Mkurugenzi, ukitoka hapa leo wakati unamalizia siku… kesho hapa pote pasafishwe. Hii kazi ya kusafisha kesho iishe,” amesema.

Amesema Serikali itashirikiana na taasisi za kifedha kusaidia wafanyabiashara wenye mikopo waliopoteza mitaji yao, pamoja na kuweka utaratibu wa kuwaongezea muda wa kurejesha mikopo hiyo na kuwezesha upatikanaji wa mikopo mipya yenye nafuu kupitia mamlaka za serikali za mitaa.

“Mkurugenzi sasa kwenye mikopo mipya nenda kaangalie una ukoko gani… tufanye kipaumbele kwa hawa ambao mtaji wao umeungua ili wapate haraka,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameagiza kuwepo kwa eneo la stendi katika mpango wa ujenzi wa soko hilo ili kurahisisha shughuli za biashara.

Kadhalika, amekemea vitendo vya ulanguzi wa vibanda katika masoko na kusisitiza kuwa vibanda vitolewe kwa wafanyabiashara halisi wanaofanya biashara.

Vilevile, amewataka wananchi kushirikiana katika kulinda amani na utulivu wa nchi, akisisitiza kuwa amani ni msingi wa shughuli zote za kiuchumi. “Ni lazima tuwe na amani kwenye nchi yetu. Kila Mtanzania awe mdau wa amani katika nchi yetu,” amesema.

Kwa upande mwingine, Waziri Mkuu amesisitiza umuhimu wa kuheshimu sekta binafsi katika kukuza uchumi wa nchi, akieleza kuwa ndiyo mhimili mkuu wa ajira kwa Watanzani












Top News