📍 Mlimba, Kilombero – Morogoro

Shamba la Chita JKT, lenye ukubwa wa ekari 12,000 zinazolimwa, limepangwa kuwa mfano wa ushirikiano kati ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na Tume ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC). 

Tangu mwaka 2021, Jeshi limekuwa likiendeleza mashamba haya kwa kutumia rasilimali za ndani, likikodisha mitambo na kusawazisha mashamba ili kuongeza tija ya uzalishaji wa mpunga.

Katika ziara yake ya hivi karibuni, Mkurugenzi Mkuu wa NIRC, Bw. Raymond Mndolwa, ametembelea maeneo ya mito yenye miundombinu ya kupeleka maji mashambani na kukutana na uongozi wa JKT katika skimu hiyo na kutoa maagizo mahsusi ya kuimarisha skimu hiyo na kuahidi kuchukua hatua za haraka ndani ya siku 14, lengo likiwa ni kuijengea uwezo CHITA JKT katika uzalishaji wa mazao.


Bw. Mndolwa amesisitiza kuwa upo umuhimu wa kutafuta mbinu ya uhifadhi wa maji, ikiwemo kujenga mabwawa, ili maji mengi yanayopotea yaweze kuhifadhiwa na kutumika kwa Umwagiliaji.Ameeleza

“Kunauhitaji wa kujengwa bwaw jipya, lijengwe kwa kutumia maji kutoka Mto Monyo, ili kusaidia kilimo cha mpunga na shughuli nyingine za matumizi ya maji kwa Chuo cha Jeshi kilichopo eneo hilo” amesema 

Mndolwa ameongeza kuwa Kutokana na changamoto za usawazishaji wa mashamba, usanifu utafanyika upya kwa kushirikisha wataalamu wa Jeshi, NIRC na Mshauri Elekezi

“Ndani ya siku 14, usanifu huo upitiwe ili kuboresha ujenzi unaoendelea na kubaini vyanzo vipya vya kujenga mabwawa” ameongeza Mndolwa 

NIRC ipo tayari kuendelea kushirikiana na Jeshi la kujenga Taifa, kuhakikisha hekari zote 12,000 zinamwagiliwa ipasavyo, na bajeti itatengwa mara usanifu utakapokamilika.

Amesisitiza kuwa maboresho ya vyanzo vya maji na upanuzi wa mashamba katika eneo hilo la JKT ni  sehemu ya mpango wa muda mrefu wa NIRC wa kuongeza tija ya uzalishaji katika kilimo cha Umwagiliaji na kwamba hatua hizo zinalenga kulifanya Shamba la Chita JKT kuwa mfano wa kitaifa wa kilimo cha kisasa, sambamba na malengo ya Dora 2050 na Mpango wa Maendeleo wa Miaka 5 wa serikali.

Naye Afisa Tawala wa Jeshi la Kujenga Taifa, Brigedia Jenerali Hassan Rashid Mabena, alisifu hatua ya NIRC kupitia Mkurugenzi Mkuu Mndolwa, kwa kutembelea na kujionea shughuli zinazofanywa na Jeshi na kuchukua hatua za haraka. 

Amesema ushirikiano huo utaliwezesha Jeshi kufikia malengo yake ya kuongeza uzalishaji wa mazao na kutatua changamoto zinazojitokeza.

Ziara ya Mkurugenzi Mkuu NIRC imeweka mwelekeo mpya wa kimkakati kwa Shamba la Chita JKT, kutoka kilimo kinachotegemea rasilimali za ndani, kuelekea kilimo cha Umwagiliaji chenye mabwawa ya kudumu na mashamba yaliyosawazishwa kitaalamu. 

Ushirikiano wa NIRC na Jeshi unatarajiwa kufanya Chita JKT kuwa nguzo ya uzalishaji wa mpunga na mazao mengine nchini Tanzania na mfano wa ushirikiano wa kitaifa katika sekta ya Umwagiliaji.





 

Waziri wa Kilimo, Mhe. Daniel Chongolo (Mb) ameelekeza mambo sita muhimu kuzingatia ili ushirika kuimarika zaidi na kuleta tija kwa wanaushirika.


Akizungumza tarehe 30 Januari 2026 jijini Dodoma wakati akizindua Bodi ya Makamishna wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC), Waziri Chongolo amesema Kamisheni ihakikishe inaleta mageuzi ya kidigitali ili takwimu sahihi zipatikane kwenye mizani ya kidigitali na kupunguza udanganyifu kwa wanachama na wakulima. 
 
Jambo la pili ameielekeza Kamisheni kuhakikisha ukaguzi unafanyika kwa vyama vyote vya ushirika nchini kila mwaka na hatua stahiki kuchukuliwa kwa wahusika wote wanaokiuka taratibu na kurudisha nyuma jitihada za maendeleo ya ushirika.  Pia, masoko ya nje yatafutwe ili bidhaa zinazozalishwa na Vyama vya Ushirika ziuzwe na kuleta tija ya mitaji.
 
Kuhusu suala la nne, Kamisheni imetakiwa kuhakikisha mali za vyama vya ushirika zinawekezwa ipasavyo ili ziweze kuzalisha na kusaidia kuleta maendeleo yanayotarajiwa na wanaushirika.  Sambamba na hilo, uadilifu, weledi na ubunifu vimetiliwa mkazo kuwa ni chachu ya kuimarisha ushirika. 
 
Aidha, jambo la mwisho ni kuhakikisha kunakuwa na ujenzi wa viwanda, upatikanaji wa huduma za bima ya mazao, huduma za matibabu na mafao ya uzeeni kwa wakulima. 

“Ni matumaini yangu kuwa Kamisheni hii itaweza kutekeleza haya kwa weledi na niwapongeze tena Wajumbe wote kwa kuteuliwa kwani tunahitaji kuleta matokeo kwa wakulima,” amesema Mhe. Chongolo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamisheni ya Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania, Bw. Abdulmajid Nsekela amemuhakikishia Mhe. Waziri Chongolo kuwa Bodi na pia kwa kushirikiana na Mrajis na Mtendaji Mkuu wa lTCDC, Dkt Benson Ndiege watatekeleza maelekezo yake katika kuhakikisha ushirika unakuwa nguzo ya uchumi shirikishi utakaochochea ajira na maendeleo ya Taifa.









 

Makamu wa Pili wa Rais wa Serikali Mapinduzi Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdullah amekutana na kuzungumza na Balozi wa Urusi nchini Mhe. Andrey Avetisyan aliyemtembelea Ofisini kwake Zanzibar kwa ziara ya kikazi tarehe 26 Januari ,2026.

Viongozi hao wamejadili masuala mbalimbali ya ushirikiano wa uwili na kutilia mkazo kuimarisha Utalii, Nishati, Elimu na Utamaduni na uhusiano wa kibiashara na kiuchumi kati ya Tanzania na Urusi.

Katika mazungumzo hayo Mhe. Hemed Suleiman Abdullah amesisitiza kuwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar iko tayari kuhakikisha mazingira wezeshi kwa wawekezaji kutoka Urusi wanaokwenda kuwekeza visiwani Zanzibar.

Naye Balozi Avetisyan ameishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa utayari wake wa kuimarisha biashara na uwekezaji kati ya Urusi na Tanzania.

Ametoa wito kwa SMZ kushiriki kikamilifu katika vikao vya Tume ya Pamoja ya Ushirikiano wa Kibiashara na Kiuchumi kati ya Urusi na Tanzania.

Awali Mhe. Balozi Avetisyan alikutana na kuzungumza na Kaimu Mkurungenzi wa Ofisi ya Mambo ya Nje Zanzibar Bw. Ali Suleyman Ali katika Ofisi hiyo.

Katika kikao hicho wamebadilishana mawazo kuhusu utekelezaji wa mipango ya pamoja na kukubaliana kuendelea na mashauriano kuhusu masuala ya ushirkiano wa uwili.









Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Clement Sangu, amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Kazi wa Qatar, Mhe. Dkt. Ali bin Saeed bin Samikh Al Marri, Jijini Riyadh, Saudi Arabia.

Katika mazungumzo ya viongozi hao, pande zote zimekubaliana kuimarisha ushirikiano katika masuala ya kazi na ajira, ikiwa ni pamoja na kubadilishana uzoefu, kukuza fursa za ajira na kulinda haki za wafanyakazi.

Vilevile, Ushirikiano huo umelenga kupanua fursa za ajira kwa Watanzania na kuendelea kuimarisha mahusiano ya kidiplomasia kati ya Tanzania na Qatar.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Clement Sangu, akizungumza na Waziri wa Kazi wa Qatar, Mhe. Dkt. Ali bin Saeed bin Samikh Al Marri, walipokutana katika kikao cha pembeni (side meeting) wakati wa mkutano wa Mawaziri wa Kazi (Global Labour Market Cinference) unaofanyika Jijini Riyadh, Saudi Arabia.
Benki Kuu ya Tanzania (BoT) leo tarehe 30 Januari 2026, imesema ina mpango wa kuuza sehemu ya hifadhi yake ya dhahabu kwa ajili ya kusawazisha mizania ya akiba ya fedha za kigeni na siyo kufadhili miradi ya kimkakati ya serikali.

Akizungumza katika mkutano na vyombo vya habari katika ofisi za BoT jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Masoko ya Fedha wa BoT, Bw. Emmanuel Akaro, ameeleza kuwa kinachotekelezwa ni mpango wa kuuza dhahabu iliyozidi kiwango kilichoidhinishwa, kwa lengola kusawazisha mizania ya akiba ya fedha za kigeni nchini.

“Sababu ya Benki Kuu kuuza dhahabu ni kujitoa kwenye vihatarishi vya kuwekeza kwenye dhahabu peke yake. Lazima tuhakikishe uwiano wa dhahabu na fedha nyingine za kigeni kwenye mizania ya Benki Kuu zinaendana na matarajio ya Bodi, matarajio ya nchi na matarajio ambayo hayatupelekea sisi kupata hasara”

Mkurugenzi huyo amefafanua kuwa wastani wa kununua dhahabu wa mwezi ni tani moja na kwa kipindi cha mizezi mitano iliyopita BoT imenunua wastani wa tani mbili,hivyo, kulazimika kuwekeza tani moja ya ziada katika fedha za kigeni mbalimbali.

“Kwa kipindi cha miezi mitano iliyopita kila mwezi tunanunua dhahabu wastani wa tani 2 kwa mwezi ambayo ni kwa mujibu wa sheria. Matarajio yetu mwanzoni yalikuwa ni kununua tani moja kila mwezi kwa hiyo tani moja inayozidi tunaitumia kusawazisha mizania ya akiba za fedha za kigeni”

“Kuna utaratibu wa namna ambavyo Benki Kuu inatoa fedha kwenda serikalini,fedha zinapitia Mfuko Mkuu na uidhinishwaji wake unakuwa umefanywa na Bunge na ukiangalia pale hakuna kipengele ambacho kinasema Benki Kuu inaweza kuuza dhahabu ili kuipatia serikali fedha kwaajili ya kufanya miradi yake”, aliongeza Bw. Akaro.

Hadi kufikia jana Januari 29, 2026, BoT ilikuwa na akiba ya fedha za kigeni yenye thamani yadola bilioni 6.52, na kati ya hizo, dhahabu inakadiriwa kuwa dola bilioni 1.2, dola za Marekani bilioni 3.8, na sarafu ya China (yuan) dola milioni 735.




Na Karama Kenyunko Michuzi Tv

SERIKALI kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imeanza utekelezaji kwa vitendo wa agizo la Rais Samia Suluhu Hassan la kuwekeza kwenye sayansi na teknolojia, baada ya kuwaaga wanafunzi 16 waliopata ufadhili wa masomo ya juu nje ya nchi kupitia mpango wa 'Samia Scholarship'

Wanafunzi hao wanaelekea katika Chuo Kikuu cha Johannesburg nchini Afrika Kusini kwa masomo yanayolenga kuzalisha wataalamu bingwa katika sayansi ya data, akili unde (Artificial Intelligence – AI) na teknolojia ya viwandani.

Akizungumza wakati wa hafla ya kuwaaga wanafunzi hao Januari 30, 2026, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda amesema ufadhili huo unalenga kuongeza idadi ya wataalamu katika maeneo ya sayansi ya data, akili unde na teknolojia ya viwanda.

“Mnakwenda Afrika Kusini kwa ufadhili wa masomo ambayo Rais Samia alituagiza nasi tunatekeleza kupitia wanafunzi hawa 16 kati ya 50 waliofanya vizuri katika mitihani ya kidato cha sita kwenye masomo ya sayansi yanayojumuisha hisabati ya juu (Advanced Mathematics),” amesema Prof. Mkenda.

Ameongeza kuwa wanafunzi hao wametoka katika shule mbalimbali zikiwemo shule za serikali, akieleza kuwa kati ya wanafunzi 50 waliochaguliwa, 16 wanaanza masomo Chuo Kikuu cha Johannesburg huku 34 wakitarajiwa kuendelea na masomo katika vyuo vikuu vya Ireland.

Prof. Mkenda amesema wanafunzi hao watanufaika na masomo ya darasani pamoja na kuunganishwa na kampuni za kiteknolojia zilizopo nchini Afrika Kusini ili kuwajengea uzoefu wa vitendo.

Amesema serikali imeahidi kuwekeza kwenye sayansi kwa lengo la kuzalisha wataalamu katika teknolojia ya tehama, sayansi ya data, akili unde, sayansi ya kompyuta na teknolojia ya viwandani.

“Adhima yetu ni kuongeza wanasayansi wabobezi katika maeneo hayo. Tutatumia mfuko wa Samia Scholarship kuwasomesha wanasayansi ili kuwafanya wabobezi ndani na nje ya nchi,” amesema.

Ameeleza kuwa serikali itaendelea kutoa ufadhili kwa wanafunzi wanaofanya vizuri katika masomo ya sayansi ili kukidhi mahitaji ya taifa katika sekta mbalimbali.

Prof. Mkenda amesema Tanzania imekuwa na uhaba mkubwa wa wataalamu wa Sayansi ya Nyuklia licha ya kuwa na madini ya urani, hali inayozuia nchi kunufaika kikamilifu na rasilimali hiyo.

“Sayansi ya nyuklia ni muhimu katika tiba, kilimo, maendeleo ya teknolojia na maeneo mengine. Ndiyo maana tumeanza kupeleka Watanzania kusoma shahada ya pili katika masuala ya sayansi ya nyuklia kupitia Tume ya Nguvu za Atomi Tanzania,” amesema.

Ameongeza kuwa kwa shahada ya kwanza, serikali inachukua wanafunzi waliofanya vizuri zaidi katika masomo ya sayansi na hesabu baada ya kumaliza kidato cha sita na kuwapeleka kusoma nje ya nchi.

Amesema kwa sasa wameanza na wanafunzi 50, ambapo baadhi wanasoma nje ya nchi na wengine wanapata ufadhili wa kusoma ndani ya nchi, akisisitiza kuwa programu hiyo inatekelezwa kwa haki na uwazi bila upendeleo.

“Hatuchagui kwa sura, tunaangalia ufaulu. Kigezo kikuu ni kufanya vizuri kitaaluma. Ninyi ni wababe ndiyo maana mmechaguliwa,” alisisitiza Prof. Mkenda.

Pia amesema serikali imeweka fedha za kuwasomesha Watanzania shahada ya pili katika vyuo vikuu mbalimbali ikiwemo Nelson Mandela Institute of Science and Technology pamoja na Chuo Kikuu cha India chenye tawi Zanzibar.

Ametoa wito kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari kuweka jitihada za makusudi katika masomo ya sayansi.

“Katika hili hakuna ujanja ujanja. Haijalishi wewe ni mtoto wa nani, ukifaulu vizuri tunaorodhesha kuanzia wa kwanza mpaka bajeti itakapoisha,” amesema.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Carolyne Nombo amesema uwepo wa wanafunzi hao ni ushahidi wa dhamira ya serikali ya awamu ya sita katika kuendeleza elimu ya sayansi na teknolojia.

“Kuwepo kwenu hapa leo ni ushahidi wa wazi wa dhamira ya serikali katika kuwekeza kwenye sekta ya elimu hususan sayansi na teknolojia,” amesema Prof. Nombo.

Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Sayansi, Dk. Amos Nungu amesema ufadhili huo utachochea maendeleo ya sayansi na teknolojia hususani katika eneo la akili unde na kutoa mtazamo mpya wa maendeleo ya sayansi nchini.

Miongoni mwa wanufaika wa ufadhili huo, Malaika Florence amesema safari yao imekuwa ndefu tangu kidato cha sita ambapo walikuwa wanafunzi 50 wa kwanza kitaifa kabla ya kuandaliwa katika Chuo Kikuu cha Nelson Mandela.

“Tumejengewa uwezo na misingi mbalimbali ikiwemo mafunzo ya kompyuta, usimamizi wa fedha na maarifa ya kuijua dunia,” amesema.

Ameongeza,“Tunalijua taifa limetuamini. Tunaahidi kusoma kwa bidii ili tuwe sehemu ya kutimiza malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050,” amesema.

Naye Simon Asilwe amesema utayari wa serikali kwao ni deni ambalo watalilipa kwa kurejesha matunda ya utaalamu watakaoupata kupitia ufadhili huo.


































Top News