Na Mwandishi wetu, Tanga.


Je umewahi kutembelea Mapango ya Amboni na kupata simulizi zake? 

Pengine kwa muda mrefu unatafuta mchumba uoe au uolewe lakini mambo kila ukiyapanga hayakai mkao ulionyooka, suluhisho la jambo hili linapatikana kwa  kutembelea mapango ya Amboni Tanga ili uweze kufanikisha lengo lako kupitia pango linaloitwa Fatuma.

Hifadhi ya Mapango ya Amboni ambayo inasimamiwa na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro yana maajabu mengi lakini mojawapo ni uwepo wa pango la Fatuma linalotumiwa na wageni mbalimbali ambao  wana shida zinazowatatiza ikiwemo suala zima la mtu  kukwama kutokuoa au kuolewa.

Muongoza watalii katika mapango hayo Muhsini Juma anaeleza kuwa watu wengi wamekuwa wakifanikiwa kupata wenza wao wanapofika katika pango la Fatuma ambalo limekuwa likitumika toka enzi za mababu kwa watu mbalimbali kufika na kuomba kupata mume au mke kwa kuishi nae kama mume na mke

“Katika miaka ya hivi karibuni kumekuwa na changamoto sana ya vijana kupata wake au waume wa kuwaoa, lakini wakifika katika pango hili na kusema nia yao na kutambika  basi wanafanikiwa na kumekuwa na shuhuda nyingi za wadau ambao wamefanikisha jambo hilo na kurudi kutupa mrejesho”,alisema Muhsin.

Umaarufu wa pango hili umewafanya wageni kwa nyakati tofauti kutembelea na kujifunza jinsi ya kufanya matambiko hayo na baada ya muda si mrefu basi baadhi hurudi kwa ajili ya shukran na inaaminika kwamba si wenyeji tu wa mkoa wa Tanga wanaotembelea mahali hapo bali pia na watu katika maeneo mengine nje ya nchi.

Muhsin anaeleza kuwa ukifika katika pango la Fatuma kama una mtu ambaye unataka kumuoa au kukuoa basi unataja jina lake na kumuita na haitochukua muda mrefu mtu huyo mwenyewe ataanza kukutafuta kwa lengo la kutaka kuoa au kuolewa.

Na kwa wale ambao hawana mtu kabisa wakifika katika mapango hayo wanachotakiwa kusema ni kwamba mimi mwaka huu nataka kuoa au kuolewa na namkusudia mtu flani, mwenye sifa Fulani... haichukui muda mrefu wanapata wenza wa kufunga nao ndoa.

Pango hili la Fatuma ambalo ni miongoni mwa mapango yaliyopo Amboni pia linatumika kwa kufanya matambiko yanayohusu masuala mbalimbali ya kijamii ikiwemo kupata mtoto, kuombea mvua inyeshe, kupata kazi na mambo mengine na ndiyo maana ukifika katika pango hilo watu kadhaa wa kadhaa hufanya maombi yao na mara nyingi hawataki waonekane zaidi ya kufuata taratibu za wenyeji wao kwa utulivu na faragha.

Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro imeweka utaratibu mahsusi wa kuhakikisha kuwa jamii ya mkoa wa Tanga na wale ambao bado wanaamini mambo hayo wanapata wasaa wa kufanya matambiko yao bila kuathiri utamaduni huo uliopo miaka na miaka.

Hayo ndiyo maajabu ya pango la Fatuma na hii inadhihirisha kwamba mwenda tezi na omo marejeo ngamani, Amboni ndiyo ngama yako ya kupata mume au mke ,usidharau mila kwani mdharau mila ni mtumwa.





 

● Rais Samia atunukiwa Tuzo Maalum ya Kiongozi Mwenye Maono

● Watalii wa kimataifa wafikia zaidi ya milioni 2.09 mwaka 2025.

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ameibuka kinara wa Tuzo za Kitaifa za Uhifadhi na Utalii (Serengeti Awards) kutokana na uongozi wake bora na wa kimkakati katika kukuza sekta ya Maliasili na Utalii kupitia jitihada zake za kutangaza vivutio vya Tanzania kimataifa.

Katika hafla ya utoaji wa Tuzo za Kitaifa za Uhifadhi na Utalii (Serengeti Awards) iliyofanyika leo Januari 31, 2026 katika Ukumbi wa Mount Meru Hotel jijini Arusha, Rais Samia alitunukiwa Tuzo Maalum ya Kiongozi Mwenye Maono (Visionary Leadership Award) kwa mchango wake mkubwa katika kukuza utalii na uhifadhi wa maliasili, hususan kupitia filamu za Tanzania The Royal Tour na Amazing Tanzania, pamoja na juhudi zake za kutafuta rasilimali fedha kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya utalii na kuimarisha uhifadhi. Tuzo hiyo ilipokelewa kwa niaba yake na Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba.

Akimwakilisha Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika hafla hiyo, Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba alisema jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita zimezaa matunda ambapo idadi ya watalii wa kimataifa imefikia 2,097,823 kati ya Januari hadi Novemba 2025, sawa na ongezeko la takribani asilimia 9.02 ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka 2024.

Waziri Mkuu aliongeza kuwa sekta ya Maliasili na Utalii inachangia takribani asilimia 21 ya Pato la Taifa, ikiwemo asilimia 17 kutoka utalii na asilimia 4 kutoka misitu na nyuki, sambamba na kutoa ajira kwa takribani watu milioni 3.

Kwa upande wake, Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji, alimpongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uongozi wake thabiti uliowezesha kuimarika kwa uhifadhi, ujenzi wa barabara na viwanja vya ndege katika maeneo ya hifadhi, hatua ambazo zimerahisisha shughuli za utalii na kuongeza mvuto wa Tanzania kimataifa.

Aidha, hafla hiyo ilihudhuriwa na shabiki wa klabu ya Manchester City ya Uingereza, Braydon Bent, ambaye alieleza kuvutiwa na uzuri wa vivutio vya Tanzania ikiwemo Serengeti na Ngorongoro pamoja na ukarimu wa wananchi, akisema safari hiyo itabaki kuwa kumbukumbu isiyosahaulika maishani mwake.

Katika hotuba yake, Waziri Mkuu alisisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi, kulinda mazingira, kuhakikisha wananchi wanaozunguka hifadhi wananufaika kiuchumi, pamoja na kuendeleza ubunifu na matumizi ya teknolojia ili kuongeza ushindani wa Tanzania katika soko la kimataifa la utalii.

Alimalizia kwa kuwakumbusha Watanzania kuwa amani ni tunu kuu ya Taifa na ni wajibu wa kila mmoja kulinda rasilimali zilizopo kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.





 

 

MKUU wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese,akizungumza wakati akifunga mafunzo ya kuwajengea uwezo madiwani wa Halmashauri ya Mji Handeni, Halmashauri ya Wilaya ya Handeni na Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi yaliyolenga kuwaimarisha katika masuala ya utawala bora, ufuatiliaji wa mapato na uelewa wa mipaka ya majukumu yao katika uendeshaji wa halmashauri.

Na Augusta Njoji

MKUU wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, amewataka madiwani wa Halmashauri ya Mji Handeni, Halmashauri ya Wilaya ya Handeni na Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi kuacha kutanguliza maslahi binafsi au ya kisiasa wanapotekeleza majukumu yao, na badala yake kuweka mbele maslahi ya wananchi na maendeleo ya halmashauri.

Nyamwese ametoa wito huo mjini Handeni wakati akifunga mafunzo ya kuwajengea uwezo madiwani, yaliyolenga kuwaimarisha katika masuala ya utawala bora, ufuatiliaji wa mapato na uelewa wa mipaka ya majukumu yao katika uendeshaji wa halmashauri.

Amesisitiza kuwa serikali haitavumilia uzembe, hujuma wala vitendo vyovyote vinavyozorotesha maendeleo ya halmashauri, akiwataka madiwani kuwa macho na kutoa taarifa kwa wakati pindi wanapobaini mianya ya upotevu wa mapato.

“Tunaomba mkawe wabunifu na mzishauri halmashauri namna bora ya kuboresha na kusimamia vyanzo vya mapato. Nyie ndio mnaoishi na wananchi; mnapobaini kapu linavuja, tuambieni linavuja wapi na nani analivujisha ili hatua stahiki zichukuliwe,” amesema Nyamwese.

Ameongeza kuwa madiwani ni macho na masikio ya serikali katika maeneo yao, hivyo wanapaswa kusimamia nidhamu ya watumishi, kuacha kufanya kazi kwa mazoea na kuchochea ushiriki wa wananchi katika shughuli za maendeleo.

Kwa upande wake, Katibu Tawala wa Wilaya ya Handeni, Margareth Killo, amesema mafunzo hayo yataongeza ufanisi na uwajibikaji wa madiwani katika kuwahudumia wananchi.

Naye, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Handeni, Amiri Mwaliko, pamoja na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi, Michael Chabai, wamesema mafunzo hayo yamewawezesha madiwani kufahamu vyema wajibu na mipaka yao, hali itakayopunguza migongano na kuongeza tija katika utendaji wa halmashauri.


Na Philipo Hassan - Arusha

Kamishna wa TANAPA, CPA Musa Nassoro Kuji, jana Januari 31, 2026 alipokea tuzo ya “Best Development Partner Supporting Tourism Development” kwa niaba ya Shirika la Korea International Cooperation Agency (KOICA), katika hafla ya utoaji wa tuzo za The Serengeti Awards zilizofanyika katika Hoteli ya Mount Meru jijini Arusha.

Tuzo hiyo alikabidhiwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abasi, ikiwa na dhima ya kutambua mchango wa Kituo cha “Serengeti Media Centre” kilichojengwa ndani ya Hifadhi ya Taifa Serengeti kwa ufadhili na ushirikiano wa Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa la Korea (KOICA).

Lengo la mradi huo ni kuboresha uzoefu wa watalii pindi watembeleapo hifadhi, hususan kituo cha “Serengeti Media Centre”, kwa kuwawezesha kupata picha mjongeo na mnato zinazoonyesha vivutio vya utalii na ikolojia ya Hifadhi ya Taifa Serengeti, hivyo kusaidia katika kuimarisha juhudi za uhifadhi kupitia teknolojia.

Pia, Kamishna Kuji alipata fursa ya kutoa tuzo kwa mshindi wa kipengele cha “Best Conservation Influencer”, ambapo mshindi alikuwa ni Nakaaya Sumari.

Tuzo za Serengeti Awards ni jukwaa adhimu ambalo limeendelea kutambua mchango wa wadau wa utalii na uhifadhi katika maendeleo ya sekta husika, huku zikichochea ubora wa huduma na ubunifu. Kupitia tuzo hizo, Tanzania inaendelea kuimarisha hadhi yake kimataifa kama kinara wa utalii wa safari na wanyamapori katika bara la Afrika na duniani kote.
















Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi-CCM, Bara, John Mongella akiwa ziarani Mkoani Shinyanga amehani msiba wa aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga,Hamis Mgeja aliyefariki dunia tarehe 03 Novemba, 2025.

Sambamba na hilo, Mongella akiwa ameambatana na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga, Mabala Mlolwa na Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mboni Mhita, ametumia nafasi hiyo kutoa salamu za pole, iliyoambatana na Dua ya kumuombea marehemu kutokana na weledi wake ndani ya CCM.




Na Seif Mangwangi, Michuzi TV, Arusha 

SERIKALI imesema imejiandaa kutokomeza kabisa migogoro ya ardhi nchini kupitia kampeni ya msaada wa kisheria ya Mama Samia Legal Aid inayotarajiwa kuzinduliwa hivi karibuni Jijini Tanga na baadae kuendelea katika Mikoa mingine.

Akizungumza Jana Januari 30, 2026 Jijini hapa wakati wa kufunga Mafunzo kwa Mawakili wa Serikali kuhusu masuala ya msaada wa kisheria (Mama Samia Legal Aid) katibu Mkuu wizara ya Katiba na Sheria, Eliakim Maswi amesema migogoro ya ardhi imekuwa tatizo kubwa nchini.

“ Katika awamu ya kwanza na ya pili ya zoezi la kampeni ya kutoa msaada wa kisheria ya Mama Samia Legal Aid, migogoro ya ardhi ilionekana kuwa kinara dhidi ya malalamiko mengi yaliyokuwa yakihitaji msaada wa kisheria,”

“ Kwa kuwa tumegundua hilo ni tatizo kubwa, Serikali hivi sasa tumejipanga kuhakikisha tunatokomeza kabisa migogoro hii na kufanya watu waishi kwa amani,” amesema.

Amesema tofauti na awamu zingine za kampeni hiyo, awamu hii migogoro itakayowasilishwa wataalam wa Sheria watahakikisha wanaifuatilia kuanzia mwanzo hadi mwisho wake Ili isiweze kujirudia kabisa.

Maswi amesema katika mafunzo ya siku tatu Jijini Arusha  waliyopewa Mawakili na wanasheria hao wa Serikali ni pamoja na kuhakikisha wanaondokana na rushwa kupitia kampeni hiyo Ili kuweza kutenda Haki Kwa wote.

Amesema Ili kuifanya kampeni hiyo kuwa endelevu na kuipa ngivu zaidi, wizara ya Katiba iliamua kushirikisha mamlaka za Mikoa pamoja na Tamisemi.

Maswi amesema hadi kufikia Juni mwaka Jana 2025, zaidi ya wananchi 4000 waliwasilisha maombi yao katika kampeni hiyo wakihitaji msaada wa kisheria na kwamba miongoni mwa migogoro iliyowasilishwa migogoro ya ardhi ilikuwa ikiongoza.

“ Migogoro iliyofuatia baada ya ardhi ni mirathi na pia changamoto ya ndoa, na ndio sababu tukaamua kuwaita wenzetu wa sekretarieti za Mikoa kwa kushirikiana na Tamisemi na baadae tutaita Halmashauri zote Kwa kuwa Hawa wote ndio wako karibu na wananchi,” amesema.

Amesema kampeni hiyo awali haikuwa ikitatua migogoro hadi mwisho kwa kuwa ilikuwa ikifanyika katika ngazi ya kitaifa lakini hivi sasa migogoro yote itamalizwa Hadi mwisho kwa kuwa itakuwa ikifanyika Kwa ngazi ya Mkoa na Serikali za mitaa

Akifunga mafunzo yaliyodumu Kwa siku tatu Jijini Arusha Katibu Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za mitaa TAMISEMI Adolf Ndunguru amesema  Mawakili hao wapewe mazingira wezeshi ya kufanyia kazi wote walioko katika sekretarieti za Mikoa na wahakikishe wanaviishi viapo vyao Kwa mujibu wa Sheria na miongozo iliyopo.

Aidha amewataka kwa namna yoyote kuepuka vishawishi vya rushwa vinavyoweza kupoteza Haki za wananchi, “ lengo kuu ni kuwarudishia wananchi tabasamu,” amesema na kuongeza:

“”Ikumbukwe kuwa Rais wetu ana nia njema na wananchi wake, ndio maana aliamua kuipa kampeni hii jina lake (Mama Samia Legal Aid) na kufikia mwezi wa sita mwaka Jana wananchi Milioni 4.1 walipata msaada, na tunatarajia kupitia kwenu wananchi wengi waweze kunufaika”amesema.

Kwa upande wake Katibu wa chama cha Mawakili wa Serikali, Wakili Rashid Mohamed Said amesema katika mafunzo hayo wameweza kufanya tathmini ya kampeni nzima iliyokuwa ikitolewa na  kujifunza njia mbadala ya kutatua migogoro inayowasilishwa.

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umemtaka Mkandarasi Kampuni ya CCC International Engineering Nigeria Ltd anayetekeleza Mradi wa Kusambaza umeme katika Vitongoji 135 vya Majimbo 9 ya uchaguzi Mkoani Ruvuma kuongeza kasi ya ujenzi ili kukamilisha Mradi huo kwa wakati.

Meneja wa Usimamizi wa Miradi ya Kusambaza Umeme REA, Mha. Deogratius Nagu ametoa maelekezo hayo Januari 31, 2026 kwa nyakati tofauti wakati wa ziara ya kukagua utekelezaji wa Mradi katika Vitongoji vya Mlimani Park na Liuli Chini Wilaya ya Songea Mkoani wa Ruvuma.

"Kasi ya utekelezaji wa mradi huu hairidhishi kwani hadi sasa Mkandarasi yupo asilimia 56 wakati alipaswa kuwa ametekeleza kwa asilimia 80 kwa maana kwamba amewasha vitongoji 43 kati ya vitongoji 135 ambavyo alitakiwa kuwasha,” amefafanua Mha. Nagu.

Mhandisi Nagu amemuelekeza Mkandarasi kumbadilisha Meneja wa Mradi, kuhakikisha anaongeza timu za mafundi na wataalam katika maeneo yote ya mradi na aongeze usambazaji wa vifaa vya mradi ikiwemo transafoma na nyaya ili afanikishe kukamilisha mradi mapema zaidi.

“Tumeongeza nguvu ya ufuatiliaji hapa na tumemueleza haturidhishwi na kazi yake; ahakikishe anazingatia maelekezo yaliyotolewa leo, tumejipanga kumsimamia kwa karibu zaidi na tunaamini hadi mwezi wa sita atakuwa amekamilisha mradi,” amesema Mhandisi Nagu.

Kwa upande wake Mhandisi wa Mradi, Erick Njau akizungumza kwa niaba ya Meneja wa Mradi, Li Hongli amesema kuchelewa kwa mradi kunatokana na kuchelewa kufika kwa vifaa vya mradi hata hivyo aliahidi kutekeleza maelekezo na kukamilisha mradi kwa wakati.

"Ni kweli hatuna changamoto zaidi ya hii ya kucheleweshewa vifaa na watoa huduma, tumepokea maelekezo na tunaahidi kuongeza kasi,” amesema Mha. Njau.

Aidha, akizungumza kwa niaba ya Msimamizi wa Miradi ya REA Mkoa wa Ruvuma, Mhandisi Zakaria Ng’okorome amesema mradi unatekelezwa kwa gharama ya shilingi bilioni 14.56 na kwamba utanufaisha wateja wa awali zaidi ya 5,400.




NA EMMANUEL MBATILO, MICHUZI TV

KLABU ya Yanga imelazimishwa kutoka sare ya 1-1 dhidi ya Al ahly ya Misri, mchezo ambao umepigwa kwenye dimba la New Aman Zanzibar.

Katika mchezo huo wa Ligi ya Mabingwa barabi Afrika hatua ya makundi, Yanga ilianza kupata bao kipindi cha kwanza kupitia kwa beki wao Ibrahim Hamad.

Yanga Sc anashika nafasi ya pili kwenye kundi lake akiwa na pointi 5 huku Al Ahly akiwa anaongoza kundi akiwa na pointi 8 wote wawili wakiwa wamecheza mechi nne.



Top News