NA EMMANUEL MBATILO, MICHUZI TV

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limepokea msaada wa gari maalum lenye maabara inayotembea kutoka Ubalozi wa Sweden, hatua inayolenga kuimarisha usimamizi na utekelezaji wa Sheria ya Mazingira nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Februari 19, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa makabidhiano hayo, Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Immaculate Semesi, amesema kuwa kabla ya kupatikana kwa msaada huo, baraza lilikuwa likitumia gharama kubwa na muda mrefu kuchukua sampuli na kuzipeleka katika maabara nyingine kwa ajili ya upimaji.

“Maabara hii inayotembea, yenye thamani ya shilingi milioni 715, italeta ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yetu kwa njia tatu kuu: kupunguza gharama, kuokoa muda, na kuongeza ubora wa maamuzi ya kitaalamu,” amesema Dkt. Semesi.

Amefafanua kuwa awali ililazimu sampuli kusafirishwa kwenda maabara zilizothibitishwa, jambo lililosababisha ucheleweshaji wa maamuzi. Kupitia maabara tembezi, upimaji sasa utaweza kufanyika papo hapo eneo la tukio.

Aidha, Dkt. Semesi amesema NEMC ina kanda 13 nchini, na matarajio ni kupata angalau magari 12 zaidi ya maabara tembezi ili kuimarisha huduma katika mikoa yote na kuhakikisha ukaguzi unafanyika kwa haraka na kwa ufanisi zaidi.

Kwa upande wake, Mratibu wa Mradi huo, Paul Kalokola, amesema gari hilo lina vifaa vya kisasa, ikiwemo droni zitakazosaidia kufikia maeneo magumu au yaliyofichika.

“Teknolojia hii itawezesha upimaji wa kisayansi kufanyika popote nchini na kusaidia maamuzi yanayotegemea ushahidi wa kitaalamu,” amesema Kalokola.

Naye Meneja wa Programu za Mazingira na Hali ya Hewa kutoka Ubalozi wa Sweden, Stephen Mwakifwamba, amesema mradi huo ulikuwa na thamani ya dola milioni tatu za Marekani. Amesema mradi huo haukujumuisha tu ununuzi wa maabara tembezi, bali pia uboreshaji wa sheria na kanuni za mazingira pamoja na kuzitafsiri kwa Kiswahili ili ziweze kueleweka kwa wananchi.

Ameishauri NEMC kuhakikisha vifaa hivyo vinatunzwa na kufanyiwa matengenezo ya mara kwa mara ili vidumu na kutoa huduma kwa muda mrefu.

Serikali ya Sweden imeahidi kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kuimarisha uhifadhi wa mazingira kwa maendeleo endelevu na ustawi wa wananchi.

Maabara hiyo imenunuliwa kupitia mradi wa miaka mitatu uliofadhiliwa na Serikali ya Sweden kupitia Shirika la Maendeleo la Sweden, uliolenga kujenga uwezo wa taasisi za serikali na binafsi katika usimamizi wa mazingira.








Na Farida Mangube, Morogoro

Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima (TEWW) imetakiwa kuimarisha misingi ya nidhamu, uwajibikaji na uwazi katika utekelezaji wa majukumu yake ili iendelee kuwa chachu ya maendeleo ya elimu endelevu nchini.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Elimu ya Msingi, Abdul Maulid, kwa niaba ya Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, wakati wa mkutano wa 16 wa Baraza la Wafanyakazi wa TEWW uliofanyika mkoani Morogoro.

Amesema kuwa licha ya changamoto zinazoikabili taasisi hiyo, watumishi wanapaswa kushirikiana kwa weledi, kuzigeuza changamoto kuwa fursa na kuimarisha ubunifu, hususani katika kukabiliana na changamoto za kifedha.

Aliishauri TEWW kupanua wigo wa utoaji wa programu na kubuni vyanzo mbadala vya mapato kupitia uandishi wa maandiko ya miradi mipya, hatua itakayosaidia kuongeza mapato ya ndani na kuimarisha utekelezaji wa majukumu yake.

Akizungumzia utekelezaji wa miradi, Maulid alitaja Programu ya Elimu Changamani kwa Vijana Walio Nje ya Shule (IPOSA) na Mradi wa Kuimarisha Ubora wa Elimu ya Sekondari kwa Njia Mbadala (SEQUIP-AEP).

Amesema TEWW, kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI, inatekeleza ujenzi katika halmashauri 30 za mikoa ya Manyara, Shinyanga, Simiyu, Singida, Pwani na Tanga.

Amebainisha kuwa jumla ya karakana 27 zimekamilika na zinawasaidia vijana walio nje ya mfumo rasmi kupata mafunzo ya ufundi, stadi za maisha, ujasiriamali pamoja na stadi za kusoma, kuandika na kuhesabu. Zaidi ya shilingi bilioni 1.55 zimetumika kukamilisha ujenzi huo.

Katika mradi wa SEQUIP-AEP unaotekelezwa kuanzia mwaka 2022 hadi 2025, jumla ya wasichana 13,272 waliokatiza masomo ya sekondari wamesajiliwa katika vituo 191 vinavyosimamiwa na TEWW. Aidha, mwaka 2025 wavulana 1,731 wamesajiliwa, sawa na asilimia 111 ya lengo lililowekwa.

Amesisitiza kuwa Baraza la Wafanyakazi lina wajibu wa kusimamia kwa umakini utekelezaji wa miradi yote ya kimkakati ili kuhakikisha matokeo yake yanawanufaisha wananchi.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa TEWW, Profesa Philipo Sanga, amesema taasisi imefanikiwa kujenga madarasa na majengo ya utawala katika mikoa 14 na kukarabati majengo katika mikoa 8, hatua inayoonesha matumizi yenye tija ya fedha za Serikali.

Ameongeza kuwa taasisi itaendelea kuendesha vikao vya Baraza kwa mujibu wa matakwa ya kisheria ili kuimarisha ushirikishwaji na utawala bora.






Na Diana Byera,Bukoba.

WAKALA wa Nishati Vijijini (REA)umemtambulisha mkandarasi wa kutekeleza Mradi wa umeme katika vitoji 474 vya mkoani Kagera kuanzia Februari 2026 hadi Februari 2029

Aidha Mkuu wa Mkoa wa Kagera Kanali Yahaya Ramadhani Kido amepokea timu ya wataalamu kutoka REA ambao waliambatana na mkandarasi anayejulikana CCC International Engineering Nigeria LTD .

Akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi huo Menaja Miradi Kanda ya Ziwa kwa niaba ya Meneja Mkuu wa REA Ernest Makale amesema Mkoa wa Kagera unavijiji 662 na vyote vimpata umeme.

Pia mkoa huo unavitongoji 3,665 na kati ya hivyo vitongoji 2029 vimepata umeme na vilivyobaki tayari Serikali imeidhinisha vitongoji 474 navyo vinaenda kupata umeme.

Amesema mradi huo utagharimu zaidi ya Sh.bilioni 66.5 na wananchi wa mkoa wa Kagera wapatao 15,396 watanufaika na mradi huo huku mradi wa kusambaza umeme wa vijiji 27 vilivyoko visiwani ukiendelea kukamilika

Ameongeza mradi huo unatarajia kutoa ajira kwa vijana na kuongeza uzoefu kwa vijana ambao wamesomea maswala ya umeme huku akitaka wananchi Kufanya uwekezaji na kujiongozea kipato mara baada ya mradi wa umeme kukamilika

Pia amesema Serikali imefanya mpango wa kuweka Transfoma kubwa katika miradi ya umeme Ili wananchi wanaotaka kufanya uwekezaji Vijijini wafanye shughuli za uwekezaji bila changamoto yeyote.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa Wa Kagera Kanali Yahaya Ramadhani Kido ametoa mwito kwa wakandarasi kutekeleza mradi huo kwa Bidiii na kasi kwa sababu mahitaji ya umeme kwa wananchi hasa vitongojini ni makubwa sana.

Amesema pia wakandarasi wanatakiwa kujitambulisha kwa uongozi wa serikali za vijiji ili kupewa ushirikiano na wenyeviti wa vijiji na wananchi wao katika swala la kulinda miundombinu na kutoa maeneo yao ya kupitsha nguzo za umeme.




Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) umeibuka mshindi wa kwanza na kutunukiwa tuzo kwa Taasisi zilizofanya vizuri katika uzingatiaji wa Sheria ya Serikali Mtandao, viwango na miongozo kwa taasisi zilizo katika ngazi ya nne ya ukomavu wa TEHAMA Serikalini.

Tuzo hiyo ilitolewa na Ridhiwani Kikwete, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, na kupokelewa na Bw. Donald Mhaiki, Mkurugenzi wa TEHAMA wa NSSF.

Hafla ya utoaji wa tuzo hiyo ilifanyika wakati wa kilele cha Kikao cha 6 cha Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA), kilichofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha International Conference Centre (AICC), jijini Arusha.

Ushindi huo unaonesha jitihada za NSSF katika kuimarisha matumizi ya TEHAMA na kuzingatia kikamilifu sheria, viwango na miongozo ya Serikali Mtandao nchini.








Makamu Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani (Mst) Mbarouk Salim Mbarouk leo Februari 19, 2026 akiwa na Mjumbe wa Tume, Mhe. Dkt. Zakia Mohamed Abubakar wamemtembelea ofisini kwake Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Mhe. Jabiri Omari Makame.


Viongozi hao wa Tume wapo mkoani humo kwa ziara ya kikazi ambapo wametembelea na kukagua maandalizi ya Uchaguzi mdogo wa Udiwani Kata ya Shiwinga, Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, Mkoani Songwe unaotarajiwa kufanyika Februari 26, 2026.








Katika kuendelea kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi, Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Songea (SOUWASA) imejidhatiti kuimarisha matumizi ya mfumo wa kidijitali unaowezesha wateja kuomba maunganisho mapya ya maji kwa urahisi zaidi bila kufika ofisini.

Hatua hiyo inalenga kupunguza usumbufu, kuokoa muda na gharama kwa wateja, sambamba na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma. Kupitia mfumo huo, mteja mpya anaweza kutuma maombi yake akiwa mahali popote, kwa kutumia simu janja, kompyuta au kifaa chochote chenye intaneti.

Mkuu wa Kitengo cha TEHAMA, Bi. Lucy Msigwa, ameeleza kuwa mteja anatakiwa kuingia kwenye tovuti ya huduma.maji.go.tz na kufuata hatua chache zilizoainishwa kwenye mfumo huo hadi kukamilisha ujazaji wa fomu ya maombi. Baada ya hapo, atawasilisha taarifa zake kwa njia ya mtandao na kuanza mchakato wa kupatiwa huduma.

Akisisitiza umuhimu wa matumizi ya teknolojia, Kaimu Meneja wa Uendelezaji Miundombinu, Mhandisi Frank Tembi, amesema mfumo huo umeboreshwa ili kuhakikisha maombi yanashughulikiwa kwa haraka na kwa uwazi zaidi. Amebainisha kuwa matumizi ya kidijitali ni sehemu ya mkakati wa mamlaka katika kuendana na kasi ya mabadiliko ya teknolojia na kuboresha huduma kwa jamii.

Naye Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mahusiano na Mawasiliano kwa Umma, Bw. Juma Mwakaje, amewahimiza wananchi kutembelea pia tovuti ya SOUWASA na kutumia kipengele cha Huduma za Haraka kuchagua Maunganisho Mapya, ambapo watapata maelekezo ya moja kwa moja ya jinsi ya kuwasilisha maombi yao.

SOUWASA imeeleza kuwa Mfumo huo ni dhamira ya taasisi katika kuhakikisha huduma za maji zinawafikia wananchi kwa urahisi, haraka na kwa kuzingatia misingi ya uwazi na uwajibikaji, Wananchi wametakiwa kuchangamkia fursa hiyo ili kunufaika na huduma bora zinazotolewa kwa njia ya kisasa zaidi.



-Ni kwa ajili ya kukamilisha Mchakato wa kumpata mkandarasi mradi wa maji kutoka ziwa Chala.

-Aitaka Wizara ya Fedha kufatuta fedha za malipo ya awali kuanza kwa ujenzi wa barabara Holili(Rotima)-Tarakea(Nayemi)

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba ameipa Wizara ya Maji kipindi cha wiki mbili kuhakikisha inakamilisha mchakato wa upatikanaji wa  mkandarasi wa ujenzi wa mradi wa maji kutoka chanzo cha Ziwa Chala.

Ametoa agizo hilo wakati akizungumza na wananchi wa kata ya Marangu-Kitowo, Wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro baada ya kupokea taarifa za ujenzi wa Mradi wa Maji kutoka chanzo cha ziwa Chala, Ujenzi wa mradi wa barabara Holili(Rotima)-Tarakea(Nayemi), pamoja kuweka jiwe la msingi la Shule ya Sekondari Stephen Moshi Technical. 

Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amesema kuwa ujenzi wa mradi huo unapaswa kuanza kutekelezwa kwani unategemewa kutatua changamoto ya upatikanaji wa maji katika Wilaya nzima ya Rombo.

 Kwa upande wake Waziri wa Maji, Jumaa Aweso amesema kuwa Wizara haitakuwa kikwazo katika utekelezaji wa mradi huo na watahakikisha katika kipindi cha siku 14 wanampata mkandarasi wa mradi huo.

Mradi wa maji ziwa Chala unatarajiwa kugharimu kiasi cha shilingi bilioni  8.66 na utanufaisha wananchi 34,104 katika vijiji 14 vya wilaya ya Rombo.

Kadhalika Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amemuagiza Waziri wa Fedha kuhakikisha anatafuta fedha kwa ajili ya kufanya malipo ya awali kwa mkandarasi ili aanze ujenzi wa mradi wa barabara Holili(Rotima)-Tarakea(Nayemi) kilomita 52.8

Mradi huo ambao utagharimu kiasi cha shilingi bilioni 28 unapita mpakani mwa Tanzania na Kenya na unategemewa kusaidia kukuza shughuli za kijamii, kiuchumi pamoja na utalii.

 Akizungumza baada ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa Shule ya Sekondari Stephen Moshi Technical ambayo itagharimu shilingi bilioni 1.6 Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amesema kuwa shule hiyo ni kielelezo cha uwepo wa kiongozi mwenye maono na mipango.

 “Ndani ya muda mchache sana zimejengwa shule zaidi ya 103 za aina hii nchi nzima” Amesema Dkt. Mwigulu.

 Mradi huo utahusisha Ujenzi wa madarasa 08, ofisi 02, chumba 01 cha TEHAMA, maabara ya kemia na baiolojia, mabweni 4 ya wasichana na wavulana, bwalo 01, karakana 01 ya magari, matundu 08 ya vyoo vya wasichana na wavulana na Kichomea taka.Pia utahusisha uchimbaji wa kisima cha maji cha ardhini, jengo la utawala na nyumba 01 ya mtumishi.









Na Oscar Assenga, TANGA

MBUNGE wa Jimbo la Tanga (CCM) Kassim Amar Makubel ameanza kugawa maftari kwa wanafunzi wa shule za Msingi ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuinua sekta ya elimu hapa nchini.

Makubel aliyasema hayo wakati wa halfa ya kuzindua zoezi la kugawa Madaftari kwa wanafunzi wa Shule za Msingi Pongwe kupitia Mpango wa Daftari la Mama Samia kwa kushirikiana na Taasisi ya Watoto Foundation ambapo mpango huo utazifikia shule zote kwenye Jimbo hilo.

Mbunge huyo alisema kwamba mpango huo ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Serikali na Rais Dkt Samia Suluhu katika sekta ya elimu kutokana na mabadiliko na mageuzi makubwa yaliyofanyika.

Alisema kwamba wakati alipoingia madarakani alikaa na kubaini vijana wengi wa shule ya msingi wanapitia changamoto nyingi hivyo akaona ni bora kila kila mzazi wa mtoto wa Jimbo hilo anayesoma shule ya msingi walau aguse maisha yake kwa kutoa madaftari matano 5 ili kuwapunguzia makali kwenye baadhi ya mahitaji.


Alieleza madaftari hayo ni sehemu ya mchango wake kurejesha shukrani kwa kumchagua katika uchaguzi mkuu uliopita na wameanza rasmi uzinduzi ambapo wataanza kugawa madaftari hayo Tarafa ya Pongwe na kasha kuelekea kwenye kata nyengine.

Aidha alisema kwamba Tarafa hiyo inayojumuisha Kata za Marungu,Kirare na Pongwe na baadae wataenda kwenye Tarafa nyengine ili kuhakikisha shule zote za misngi zinafikiwa na kuwagusa.



Alisema keamba mabadiliko hayo yaliyofanywa na Rais Dkt Samia Suluhu katika sekta ya elimu wakati alipoingia madarakani ni kuona elimu walionayo haikizi mahitaji ya sasa na wanatakiwa kuendana na mabadiliko kwenye mitaa ya elimu ya sasa na sasa watoto watasoma darasa la kwanza mpaka la sita.



Aidha alisema mabadiliko hayo machache ikiwemo mkondo wa amali ambao ni muhimu kwa ajili ya kuwapatia ujuzi watoto wanapomaliza shule jambo ambalo litasaidia kuongeza wataalamu mbalimbali ambao watakuwa na mchango mkubwa wa kuweza kujiajiri na kuweza kujiendeleza kwenye vyuo vya kati

“Kutokana na mabadiliko hayo makubwa ya kielimu hapa nchi na hakuna malipo hivyo tuwahimize watoto waende shule pamoja na kufuatilia maendeleo yao na tuhudhurie vikao”Alisema .



Awali akizungumza Mwalimu Mkuu Msaidizi wa shule ya Pongwe Mchanganyiko Abubakari Sadik alimshukuru Mbunge huyo kwa kuwapelekea msaada huo madaftari ambayo yamekuja kutatua changamoto ya watoto ambao hawana uwezo wa kununua madaftari kwa wakati .

"Ukosefu wa daftari ni kwamba wanafunzi asipokuwa na madaftari anakosa kumbukumbu ya kusoma kipindi anapofikia kwenye mtihani yake hivyo msaada huu umeenda kutatua changamoto ya kila mmoja kutokana na wazazi wa watoto wengine wako mbali na inakuwa vigumu kuwa na madaftari kila wakati”Alisema

Alisema kwamba shule hiyo imekuwa ikifanya vizuri katika taaluma na wamekuwa na mwendelezo mzuri wa wanafunzi katika madarasa ya mitihani ya darasa la nne.

Aliongeza kwamba changamoto ambazo zinawakabili ni upungufu wa madarasa unaotokana na ongezeo la uandikishaji wanafunzi kila mwaka na wale wanaohamia kutoka maeneo mengine huku akieleza jambo linguine ni bima za afya kwa wanafunzi wenye mahitaji maalumu.

“Tunamshukuru Mhe Mbunge Wetu kwa kutupelekea wadau wenye kuwasaidia madaftar mchango huo umewapa faraja kubwa na matumaini motisha mpya kwa watoto wao kuonyesha dhamira ya kweli kujenga jamii inayojali na kuthamini kila mtoto bila ubaguzi”Alisema

Hata hiyo alitoa shukrani zake kwa Rais Dkt Samia Suluhu katika kukuza na kutoa kipaumbeme kwenye elimu jumuishi na kupitia uongozi wake fursa za elimu zinaendelelea kuimarishwa na kuwafikia hata wenye mahitaji maalumu.

Naye kwa upande wake Mkurugenzi wa Taasisi ya Watoto Foundation Ally Yakub Pingizi alisema taasisi hiyo imezindua mpango unaoitwa Daftari la Mama Soma na Samia ikiwa ni kipaumbele kuhakikisha wanafunzi hawana sababu ya kutoroka shule ikiwa hana vitendea kazi cha shule.

Alisema kwamba wao wamekuja na mpango wa daftari la mama soma na samia ikiwa ni kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Rais Dkt Samia Suluhu katika kuboresha sekta ta elimu na amefanya maboresho makubwa kwa kujenga miundombinu ya elimu, nyumba za walimu,mabweni na vyoo.


Alisema kwamba taasisi hiyo kupitia mpango huo wameona wao waunge mkono kwa kutoa vifaa hivyo vitendea kazi na kuwatia moyo watoto wa kike waweze kusoma kwa hari na moyo ili kuepuka kujiingiza kwenye vishawishi na watoto wa kike na hivyo kusoma kwa bidii pamoja na kupunguza utoro shuleni hatua itakayochochea ufaulu.
 







Top News