Na Said Mwishehe,Michuzi TV

HATIMAYE Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi mahiri wa Rais Dk.Samia Suluhu Hassan imetangaza rasmi kwamba kuanzia Julai 1 mwaka huu wa 2025 nchi yetu ya Tanzania itaanza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Wakati utekelezaji huo ukitarajiwa kuanza tarehe hiyo ya Julai 1, tayari upo msingi imara wa kisera, kitaasisi na kiutekelezaji unaolenga kuharakisha mageuzi ya kiuchumi, kijamii na kiutawala kwa miongo ijayo. 

Katika kikao chake kilichofanyika Dar es Salaam hivi karibuni chini ya Mwenyekiti wake, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Tume ya Taifa ya Mipango iliidhinisha miongozo na mifumo muhimu ya kusimamia utekelezaji wa Dira 2050 pamoja na kuelekeza kuharakishwa kwa miradi mikubwa ya kimkakati itakayokuwa nguzo kuu ya ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Pamoja na kuidhinisha Mwongozo wa Kitaifa wa Mipango, Mwongozo wa Kitaifa wa Uidhinishaji wa Miradi ya Maendeleo, Mwongozo wa Kitaifa wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Miradi ya Maendeleo na Mkakati wa Mawasiliano wa Dira 2050, Tume imeweka msisitizo maalum katika utekelezaji wa miradi mikubwa ya uwekezaji inayotarajiwa kuchochea mabadiliko ya kimuundo katika uchumi wa Tanzania.


Miradi hiyo ni pamoja na Mradi wa Kuchakata Gesi Asilia kuwa Kimiminika (LNG), Mradi Unganishi wa Chuma cha Liganga na Makaa ya Mawe ya Mchuchuma, Mradi wa Kabanga Nickel pamoja na Kiwanda cha Usafishaji Kahama, na Mradi wa Magadi Soda wa Engaruka. 

Kwa pamoja, miradi hiyo inawakilisha uwekezaji wenye thamani ya zaidi ya shilingi trilioni 120, sawa na takribani dola za Marekani bilioni 47.

Miradi hiyo imeainishwa kama sehemu muhimu ya utekelezaji wa Dira 2050 kwa sababu ina uwezo wa kuvutia uwekezaji mkubwa wa ndani na nje, kuongeza ajira, kuimarisha mapato ya Serikali, kukuza mauzo ya nje, kuongeza matumizi ya teknolojia za kisasa na kuimarisha ushindani wa Tanzania katika uchumi wa kikanda na kimataifa.

Mradi wa LNG unatarajiwa kuwa kichocheo kikubwa cha ukuaji wa sekta ya nishati na mapato ya fedha za kigeni. 

Liganga na Mchuchuma vinatarajiwa kuweka msingi wa maendeleo ya viwanda kwa kuongeza uzalishaji wa chuma na nishati nchini. Kabanga Nickel inaipa Tanzania nafasi ya kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kijani unaochochewa na ongezeko la mahitaji ya madini muhimu kwa utengenezaji wa betri na teknolojia za nishati safi duniani. 


Nayo Engaruka inafungua fursa mpya katika sekta ya kemikali na viwanda vinavyotegemea malighafi za ndani.

Kwa kuzingatia malengo ya Dira 2050 ya kufikia uchumi wa takribani dola trilioni moja, miradi hiyo siyo uwekezaji wa kawaida bali ni injini za mageuzi ya kiuchumi. 

Hivyo uamuzi wa Tume ya Taifa ya Mipango wa kuipa kipaumbele utekelezaji wake unaashiria dhamira ya Serikali ya kuhakikisha Dira 2050 inatafsiriwa katika matokeo halisi yatakayoongeza tija, ajira, ustawi wa wananchi na ushindani wa Taifa katika miaka ijayo.

Pamoja na hayo ukweli ni kwamba kuanza kwa utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inaonesha dhamira,kiu na shauku ya Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kuona nchi yetu inapiga hatua zaidi katika kuleta maendeleo, kuboresha hali za maisha ya wananchi na kubwa zaidi kuifanya Tanzania kuwa injini ya kukuza uchumi wake kupitia rasilimali zake .

Unapoiangalia Dira ya Taifa ya Maendeleo unaiona Tanzania tuitakayo na safari ya kuelekea huko inaanza sasa. Hongera Serikali ya Awamu ya Sita kwa hatua hii inayowasha taa ya kijani yenye matumaini makubwa kwa Watanzania.

Lakini kwa muda mrefu Watanzania tumekuwa tukiitamani Tanzania itakayokuwa na uwezo mkubwa wa kuajiri watu wake kupitia sekta mbalimbali na katika Dira hiyo imeeleza kwa kina namna ambavyo nchi inavyokwenda kuimarisha sekta hizo kama mkakati wa kutengeneza fursa za ajira kwa Watanzania.

Kwa mfano Tume ya Taifa ya Mipango chini ya Rais Dk.Samia Suluhu Hassan katika kikao chake cha Mei 26 pamoja na mambo mengine pia imeidhinisha sekta za kipaumbele 12 wakati wa utekelezaji wa dira hiyo.

Sekta hizo ni ya kilimo idadi ya viashiria vya upimaji katika mabano ni (15), viwanda na ujenzi (10), Madini na Nishati(10), Utalii(5), michezo na Sanaa(9), sekta ya ubunifu na maudhui ya kidigitali(2) wakati sekta ya miliki ,aridhi na maendeleo ya miji(13)

Pia sekta nyingine ni biashara na uwekezaji(12), Elimu(54), hifadhi za jamii,kazi na ustawi wa jamii(34), uchumi wa bluu(18) pamoja na sekta ya Sayansi,teknolojia,ubunifu na uchumi wa digitali(24).

Unapoangalia sekta hizo ambazo zimepewa kipaumbele katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 utabaini mkakati uliopo kama nchi ni kuhakikisha Tanzania inaendelea kufungua fursa zaidi ambazo kila mmoja atashiriki katika shughuli za kiuchumi na hatimaye kwa pamoja kubadilisha maisha yetu kutoka tuliyonayo sasa na kuwa na maisha bora zaidi.

Na kwa kuwa dira hiyo imelenga kubadilisha maisha yetu ni matumaini yangu wananchi wote na wa rika na kada zote tunaowajibu wa kuungana na Rais Dk.Samia na Serikali anayoiongoza katika kuwa sehemu ya safari ya kutekeleza dira hiyo ambayo ikifanikiwa kizazi kilichopo sasa na kijacho kitakuwa kwenye ile nchi ya ahadi ya asali na maziwa.

Kupitia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inaonesha jinsi ambavyo inakwenda kuinua uchumi wa mtu mmoja mmoja na lengo ni kuwezesha pamoja na kuwa na ukuaji wa uchumi kwa ujumla kama Taifa lakini pia uchumi wa kila mmoja wetu nao ukue.Ndio mpango uliopo.

Binafsi sina shaka na Rais Dk.Samia katika kusimamia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwani kwa dhamira yake na utashi wake ndio aliyetoa maelekezo ya kuandikwa kwa Dira hiyo kazi ambayo ilifanyika kwa weledi mkubwa na kupita katika hatua mbalimbali na hatimaye sasa utekelezaji wake unakwenda kuanza rasmi.

Hata hivyo nitoe rai kwa Vyama vya siasa nao wanapaswa kuwa sehemu ya kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa dira hiyo.Ni matumaini yangu kama ilivyo kwa CCM Ilani yake imeakisi kwa kiasi kikubwa yaliyomo katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Hivyo kwa vyama vya siasa vya upinzani kuakisi yaliyomo katika Dira hiyo kupitia Ilani zao.Lakini kwa kuwa utekelezaji wa dira unaanza Julai 1,2026 ni vema wanasiasa wetu bila kujali itikadi ya vyama wakaungana na Watanzania wote kuitekeleza dira hiyo.


Simu 0713833822


Mwisho



 

Kamati ya Kudumu ya Bunge inayosimamia masuala ya Utawala, Katiba na Sheria imeeleza kuridhishwa na hatua zilizofikiwa katika utekelezaji wa miradi ya uwekezaji ndani ya Eneo Maalum la Kiuchumi la Bagamoyo – BEMC. Kauli hiyo imetolewa baada ya kamati kufanya ziara ya ukaguzi ili kujionea maendeleo ya shughuli mbalimbali zinazosimamiwa na Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania, TISEZA.

Eneo la BEMC lilianzishwa kisheria kupitia Tangazo la Serikali Na. 123 la tarehe 24 Mei 2013. Lina jumla ya hekta 9,800, ambapo hekta 887 zimetengwa mahsusi kwa ajili ya Bandari ya kisasa ya Mbegani. Sehemu iliyobaki, yenye hekta 8,903, inatumiwa kwa shughuli za uwekezaji. Mradi huu unatajwa kuwa wa kimkakati kitaifa na unalenga kukuza sekta ya viwanda, biashara na uchumi kwa ujumla.

Katika Mpango wa Maendeleo wa Taifa, BEMC umetambuliwa kama moja ya nguzo zitakazosaidia Tanzania kufikia lengo la kuwa na uchumi wenye thamani ya dola trilioni moja ifikapo 2050. Kufikia Mei 2026, wawekezaji 24 tayari walikuwa wameshapatiwa maeneo na kuanza utekelezaji wa miradi yao. Miradi hiyo ipo katika hatua tofauti kama ujenzi wa viwanda, mabanda ya uzalishaji, uzio pamoja na miundombinu wezeshi.

Wakati wa ziara hiyo, Kamati ilisema imefurahishwa na kasi ya ujenzi na uwekezaji unaoendelea. Miongoni mwa miradi iliyotajwa kuvutia ni kiwanda cha Sinovest Industry Investment Limited kitakachozalisha nguo na bidhaa za nguo. Kiwanda hicho kimejengwa kwenye eneo la mita za mraba 210,080, sawa na hekta 21. Mpaka Mei 2026, uwekezaji uliofanyika ulifikia dola milioni 7 za Marekani, sawa na zaidi ya shilingi bilioni 21. Kinatarajiwa kuanza uzalishaji rasmi mwishoni mwa Juni 2026.

Kukamilika kwa kiwanda hicho kutaleta ajira nyingi. Awamu ya kwanza itazalisha ajira 1,000 za moja kwa moja, na awamu ya pili itaongeza ajira 500. Kiwanda kitatumia mashine za kisasa kuzalisha nguo zenye ubora wa kimataifa kwa ajili ya masoko ya Marekani na Ulaya.

Uwekezaji wa aina hiyo unachangia kwa kiasi kikubwa pato la Taifa, unaongeza thamani ya bidhaa za viwandani, pamoja na kuboresha kipato cha wananchi wa Bagamoyo, Mkoa wa Pwani na Tanzania nzima.

TISEZA inalenga kuhakikisha maeneo yote maalum ya uwekezaji yanatumika kikamilifu ili kuvutia mitaji na kuleta tija kwa wananchi. Lengo ni kuwafanya Watanzania wanufaike na fursa za uwekezaji katika sekta mbalimbali. Uwekezaji unabaki kuwa chombo muhimu cha kutoa ajira, kuvutia mitaji kutoka nje, kuhamisha teknolojia na kuimarisha msingi wa viwanda nchini.

Maendeleo yanayoonekana BEMC yanaonyesha nia ya dhati ya Serikali katika kuboresha mazingira ya uwekezaji na kusukuma utekelezaji wa miradi mikubwa yenye maslahi mapana kwa wananchi na Taifa.







-Pia yabainisha mkakati wa mageuzi katika mifumo ya utawala na utumishi wa umma

-Utekelezaji Dira 2050 kuanza kutekelezwa rasmi kuanzia Julai 1, 2026


Na Said Mwishehe,Michuzi TV


TUME ya Mipango ya Taifa imeidhinisha miongozo minne itakayotumika katika kusimamia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 utakaoanza Julai 1 mwaka 2026.

Akizungumza leo Mei 31 katika mkutano wa waandishi wa habari uliofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam,Waziri wa Mipango na Uewekezaji Profesa Kitila Mkumbo amesema miongozo hiyo imetolewa baada ya Tume ya Taifa ya Mipango chini ya Mwenyekiti wake Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kufanya kikao Mei 26 mwaka huu.

“Katika kikao hicho, pamoja na mambo mengine, Tume ya Taifa ya Mipango ilijadili na kuidhinisha miongozo/mikakati minne itakayotumika katika kusimamia tekelezaji wa Dira 2050 utakaonza Julai 1, 2026.”

Profesa Mkumbo ameitaja miongozo hiyo ni Mwongozo wa Kitaifa wa Mipango,Mwongozo wa Kitaifa wa Uidhinishaji wa Miradi ya Maendeleo, Mwongozo wa Kitaifa wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Miradi ya Maendeleo,Mkakati wa Mawasiliano wa Dira 2050 wa Miaka Mitano 2026/27 - 2030/31.

“Ilipojadili Muongozo wa Kitaifa wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Miradi ya Maendeleo, Tume ya Taifa ya Mipango iliidhinisha maeneo makubwa matatu ya kimkakati yanayohitaji mageuzi yenye viashiria vya upimaji 142.

“Maeneo haya na idadi ya viashiria vyake ya upimaji ni Mageuzi katika mifumo ya utawala na utumishi wa umma (Governance and civil service reforms, viashiria 13), Mageuzi katika uwekezaji na uzalishaji (structural transformation for investment, infusion and productivity, viashiria 53) pamoja na Mageuzi katika maendeleo ya kijamii, kiuchumi na mazingira (socio economic outcomes, viashiria 76)

Ameongeza pia Tume ya Taífa ya Mipango ilidhinisha sekta za kipaumbele 12 kama zilivyainishiwa katika Mpango wa Nne wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka
Mitano yenye viashiria vya upimaji 206

Amefafanua katika sekta ya kilimo idadi ya viashiria vya upimaji katika mabano ni 15, viwanda na ujenzi (10), Madini na Nishati(10), Utalii(5), michezo na Sanaa(9), sekta ya ubunifu na maudhui ya kidigitali(2) wakati sekta ya miliki ,aridhi na maendeleo ya miji(13)

Pia katika sekta ya biashara na uwekezaji(12), Elimu(54), hifadhi za jamii,kazi na ustawi wa jamii(34), uchumi wa bluu(18) pamoja na sekta ya Sayansi,teknolojia,ubunifu na uchumi wa digitali(24).

Akieleza zaidi Profesa Mkumbo ameeleza pia Tume ya Taifa ya Mipango ilielekeza kuwa Sekretariati ya Tume ijielekeze na kujikita katika kusimamia utekelezaji wa mipango ya maendeleo.

Aidha, katika kumarisha simamizi wa utekelezaji wa mipango ya maendeleo, Mwenyekiti
wa Tume alielekeza kuwa, wakati ambapo Tume haikutani katika vikao vya kawaida chini yake, wajumbe wa Tume watajigeuza kuwa Ofisi ya Usimamizi wa Utekelezaji wa Mipango (Delivery Bureau) na vikao vyake vitasimamiwa na
Makamu Mwenyekiti wa Tume.

Ameongeza Tume ya Taifa ya Mipango ilielekeza kukamilishwa kwa haraka kwa majadiliano kati ya Serikali na wawekezaji kuhusu miradi ya kimkakati ya uwekezaji inayotarajiwa kujenga msingi ya kukuza uchumi na kuchochea ajira kama sehemu muhimu ya utekelezaji wa Dira 2050 na Mpango wa Nne wa Taifa wa Maendeleo ya Miaka Mitano (2026/27 - 2030/31).

Amitaja miradi hiyo ni Mradi unganishi wa chuma cha Liganga na makaa ya mawe ya Mchuchuma, Mradi wa magadi soda wa Engaruka, Mradi wa kuchakata gesi asilia kuwa kimiminika (LNG), Mradi wa nikeli wa Kabanga (Kabanga Nickel Project) na kiwanda cha usafishaji cha Kahama.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Mhe. Profesa Kitila Alexander Mkumbo akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu kuanza Utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 (DIRA2050), tarehe 31 Mei, 2026 Ikulu, Dar es Salaam.



Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Arusha, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Zauda Mohamed, ameongoza mafunzo maalum kwa walimu wa vyuo vya udereva jijini Arusha, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuimarisha ubora wa mafunzo ya udereva na kuongeza usalama barabarani Pamoja na Kuimarisha matumizi ya Tehama katika Usimamizi wa vyuo hivyo.

Mafunzo hayo yanaendelea kutolewa katika Chuo cha Ufundi Arusha (Arusha Technical College - Arusha Tech), ambapo walimu hao wanapatiwa ujuzi na mbinu za kisasa zitakazowawezesha kuandaa madereva wenye sifa, weledi na uelewa unaokidhi mahitaji ya sheria, kanuni na taratibu za usalama barabarani za sasa.

Akizungumza baada ya mafunzo hayo, ACP Zauda Mohamed amesema lengo la Kikosi cha Usalama Barabarani ni kuhakikisha walimu wa vyuo vya udereva wanakuwa na uwezo wa kuzalisha madereva wenye viwango vinavyokubalika kitaifa na kimataifa.

“Tunataka kuona madereva wanaopata mafunzo kutoka kwa walimu hawa wanakuwa na sifa stahiki na kuzingatia sheria za usalama barabarani. Hii itasaidia kupunguza ajali za barabarani na hatimaye kuokoa maisha ya wananchi,” amesema ACP Zauda.

Ameongeza kuwa kikosi hicho kinaendelea kuweka mkazo katika utoaji wa elimu na mafunzo kwa wadau mbalimbali wa sekta ya usafirishaji ili kuhakikisha ajali za barabarani zinapungua kwa kiwango kikubwa, na ikiwezekana kutokomezwa kabisa.

Pia amewataka walimu hao kuendelea kuboresha mbinu za ufundishaji na kuzingatia mabadiliko ya teknolojia pamoja na mahitaji ya soko la ajira, akibainisha kuwa kwa sasa mahitaji ya madereva wenye taaluma na ujuzi wa kutosha yanaongezeka ndani na nje ya nchi.

Kwa upande wao, baadhi ya walimu wa vyuo vya udereva waliohudhuria mafunzo hayo wamelishukuru Jeshi la Polisi kupitia Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Arusha kwa kuendelea kuwawezesha kitaaluma mara kwa mara.

Wamesema mafunzo hayo yanawajengea uwezo wa kufundisha kwa viwango vya juu zaidi na kuwasaidia kuzalisha madereva wenye umahiri unaokidhi vigezo vya kitaifa na kimataifa.






WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Jumapili Mei 31, 2026 amekagua ujenzi wa Barabara ya Noranga (Doroto)–Itigi (Mlongojii) yenye urefu wa kilomita 25 inayojengwa katika Halmashauri ya Itigi, Wilaya ya Manyoni mkoani Singida kwa gharama ya shilingi bilioni 29.6.

Akipokea taarifa ya utekelezaji wa mradi huo kutoka kwa Mkurugenzi wa Miradi wa Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS), Mhandisi Japherson Nnko, Dkt. Mwigulu alielezwa kuwa hadi Mei 30, 2026 mradi huo umefikia asilimia 83.25 ya utekelezaji ambapo kilomita 20.2 zimekamilika kwa kiwango cha lami huku kilomita 4.8 zilizobaki zikiwa zimejengwa hadi tabaka la juu la msingi na zinatarajiwa kukamilika Juni 30, 2026.

Mhandisi Nnko alisema kipande hicho ni sehemu ya Barabara ya Mbeya–Chunya–Makongolosi–Rungwa–Itigi–Mkiwa yenye urefu wa kilomita 524 inayounganisha mikoa ya Mbeya, Singida na Tabora na ambayo inatarajiwa kuimarisha usafirishaji wa watu, bidhaa na mazao katika ukanda huo.

Alisema mradi huo unagharamiwa kwa asilimia 100 na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na unatekelezwa na Kampuni ya China Henan International Cooperation Group Co. Ltd (CHICO) kutoka China kwa gharama ya shilingi 29.6 bila VAT.

Aidha, alisema kazi za ujenzi zilianza Septemba 16, 2022 na zinatarajiwa kukamilika Agosti 7, 2026 baada ya mkandarasi kuongezewa muda wa utekelezaji kwa mujibu wa mkataba.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, hadi Mei 30, 2026 mkandarasi alikuwa amelipwa shilingi bilioni 12.9 na alikuwa anadai shilingi bilioni 3.84. Aidha, Mhandisi Mshauri alikuwa amelipwa shilingi bilioni 1.49 na anadai shilingi milioni 586.6.

Pia, wananchi 578 ambao mali zao ziliathiriwa na mradi huo wamelipwa fidia ya jumla ya shilingi milioni 721.4 kwa mujibu wa sheria.

Katika utekelezaji wake, mradi huo umezalisha ajira 305 ambapo ajira 278 sawa na asilimia 91 zimetolewa kwa wazawa na ajira 27 sawa na asilimia 9 zimetolewa kwa wageni.













Serikali ya Tanzania imesaini mkataba na Kampuni ya Lindi Jumbo Limited kwa ajili ya kuwezesha ushiriki rasmi wa Serikali katika Mradi wa uchimbaji wa madini ya kinywe wa Lindi Jumbo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, hatua inayotajwa kuwa mafanikio makubwa kwa sekta ya madini na mkakati wake kupitia ajenda ya madini nchini.

Hafla ya utiaji saini iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi, imeiwezesha Serikali kupata asilimia 16 ya hisa huru zisizohafifishwa thamani katika mradi huo, huku Lindi Jumbo Limited ikibaki na umiliki wa asilimia 84.

Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde, alisema makubaliano hayo ni hatua ya kihistoria katika kuhakikisha Watanzania wananufaika moja kwa moja na rasilimali za taifa kupitia ushiriki wa Serikali katika uwekezaji wa madini.

Kwa mujibu wa makubaliano hayo, Serikali itashiriki katika mradi bila kubeba gharama za awali za uwekezaji, huku ikipata gawio, kushiriki katika maamuzi ya kimkakati pamoja na kuongeza usimamizi wa mapato yatokanayo na madini.

Mheshimiwa Mavunde alisema makubaliano hayo yanaonesha mabadiliko ya namna Tanzania inavyosimamia rasilimali zake za madini, akisisitiza kuwa nchi inapaswa kuondokana na utegemezi wa kuuza malighafi pekee.

“Serikali chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan imeendelea kuimarisha taswira ya Tanzania kama eneo tulivu na rafiki kwa wawekezaji,” alisema. “Kupitia sheria zilizo wazi, taasisi zinazoendelea kuimarika na dira ya muda mrefu ya uchumi, wawekezaji sasa wanaiona Tanzania siyo tu kama chanzo cha madini, bali mshirika wa kuaminika katika uwekezaji wenye usawa na endelevu.”

Waziri huyo alieleza kuwa Kinywe imeendelea kuwa madini muhimu duniani kutokana na matumizi yake katika utengenezaji wa betri za magari ya umeme, teknolojia za nishati safi na mabadiliko ya mfumo wa matumizi ya nishati duniani.

Aliitaja Kinywe kama “dhahabu nyeusi” ya uchumi wa kisasa, akisema uchumi wa dunia utaendelea kutegemea madini mkakati yanayochochea maendeleo ya teknolojia na mifumo ya nishati ya kijani.

Kwa mujibu wa Mheshimiwa Mavunde, Mradi wa Lindi Jumbo ni miongoni mwa miradi yenye kiwango cha juu zaidi cha ubora wa kinywe duniani, ukiwa na wastani wa asilimia 17.9 ya Total Graphitic Carbon (TGC), hali inayoufanya kuwa moja ya migodi bora zaidi ya kinywe barani Afrika. Mradi huo unatarajiwa kuzalisha takribani tani 40,000 za kinywe kwa mwaka katika kipindi cha miaka 24 ya uhai wa mgodi.

Waziri huyo pia alisisitiza dhamira ya Serikali katika kuendeleza uchumi wa viwanda na kuongeza thamani ya madini, akisema Tanzania inalenga kuhamasisha uwekezaji katika uchakataji wa madini, utengenezaji wa betri na viwanda vinavyotegemea kinywe pamoja na madini mengine ya kimkakati.

Akihitimisha hotuba yake, Mheshimiwa Mavunde alisema Tanzania imejipanga kujenga sekta ya madini ya kisasa, thabiti na yenye ushindani wa kimataifa inayozingatia uwazi, uhakika na ushirikiano wa muda mrefu.

Alisema makubaliano hayo yanaashiria enzi mpya ya ushirikiano kati ya Serikali, wawekezaji na wananchi, yakionyesha kuwa uwekezaji, uzalendo na ukuaji wa uchumi vinaweza kwenda sambamba.

“Utajiri wa madini wa Tanzania lazima ugeuzwe kuwa ajira, viwanda, maarifa na matumaini kwa vizazi vijavyo,” alisema.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Lindi Jumbo, Andrew Cunningham, alisema utiaji saini wa makubaliano hayo ni ishara ya mafanikio ya safari ndefu ya maendeleo ya mradi huo pamoja na mwanzo wa hatua mpya ya ushirikiano na ukuaji wa sekta ya kinywe nchini Tanzania.

Bwana Cunningham alisema Mradi wa Lindi Jumbo ulianza zaidi ya miaka kumi iliyopita, huku shughuli za utafiti wa madini zikianza mwaka 2015 kwa lengo la kufungua fursa ya utajiri wa grafiti nchini Tanzania.

Alisema tangu wakati huo mradi huo umepitia hatua mbalimbali zikiwemo utafiti, tafiti za kitaalamu, upatikanaji wa fedha, ujenzi na uzalishaji hadi kufikia kuwa moja ya migodi bora ya kinywe duniani.

“Lindi Jumbo unakadiriwa kuwa na maisha ya mgodi ya miaka 24, huku ukiwa na uwezekano mkubwa wa kuongeza shughuli za uzalishaji hadi zaidi ya miaka 50 kutokana na utafiti unaoendelea,” alisema Bwana Cunningham. “Thamani ya mradi huu haipo tu katika muda wake mrefu wa uzalishaji, bali pia katika ubora mkubwa wa madini yake unaouweka katika nafasi nzuri katika soko la kimataifa la madini mkakati.”

Alisema kinywe imeendelea kuwa madini muhimu katika uchumi wa kisasa kutokana na matumizi yake katika shughuli za viwanda, teknolojia za kisasa na mifumo mipya ya nishati.

Kuhusu uzalishaji, mkurugenzi huyo alisema, mwaka 2025 mgodi huo ulisindika karibu tani kavu 170,000 za madini ghafi na kuzalisha tani 16,421 za kinywe yenye kiwango cha ubora kati ya asilimia 94 na 96 TGC.

Aliongeza kuwa mradi huo ulichimba zaidi ya tani 500,000 za mchanga na miamba katika kipindi hicho, huku oda za mauzo zilizothibitishwa zikizidi tani 27,800.

Bwana Cunningham pia alieleza mchango wa mradi huo kwa uchumi wa Tanzania, akisema kampuni ilitumia shilingi bilioni 57.5 kwa wazabuni wa ndani kati ya mwaka 2024 na 2025, ambapo asilimia 91 ya manunuzi yote yalielekezwa kwa kampuni za Kitanzania.

Aidha, kampuni hiyo ilichangia zaidi ya shilingi bilioni 11.3 kupitia mrabaha, kodi na malipo mbalimbali ya kisheria kwa Serikali.

Kwa mujibu wa Bwana Cunningham, mradi huo pamoja na wakandarasi wake unaajiri watu 280, ambapo zaidi ya asilimia 95 ni Watanzania, huku zaidi ya nusu ya wafanyakazi wakitoka vijiji vinavyozunguka Wilaya ya Ruangwa.

Pia alieleza juhudi za kampuni katika uwekezaji kwa jamii, akibainisha kuwa zaidi ya shilingi milioni 162 zimetengwa kwa ajili ya programu za uwajibikaji kwa jamii katika sekta za afya, elimu na maendeleo ya jamii.

Miongoni mwa miradi hiyo ni ujenzi wa zahanati katika Kijiji cha Namilema kwa lengo la kuboresha huduma muhimu za afya kwa wananchi wa maeneo yanayozunguka mradi huo.

Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde (wa pili kushoto), akishikana mikono na Mkurugenzi wa Lindi Jumbo, Andrew Cunningham, baada ya hafla ya utiaji saini wa makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Lindi Jumbo Limited kuhusu ushiriki wa Serikali katika Mradi wa kinywe wa Lindi Jumbo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi. Wanaoangalia kutoka kulia ni Mwakilishi kutoka Ofisi ya Msajili wa Hazina, Emmanuel Luvanda; Mwakilishi wa Gemcorp, William Binedell; na Mwanasheria na Katibu wa Kampuni ya Lindi Jumbo, Ephraim Mrawa.

Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde (wa pili kushoto), akiwa na, kutoka kushoto, Mkurugenzi wa Lindi Jumbo, Andrew Cunningham; Mwanasheria na Katibu wa Kampuni ya Lindi Jumbo, Ephraim Mrawa; pamoja na Mwakilishi wa Gemcorp, William Binedell, wakionesha hati za mikataba, baada ya utiaji saini wa makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Lindi Jumbo Limited kuhusu ushiriki wa Serikali katika Mradi wa kinywe wa kampuni hiyo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi.


Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde, akisaini nyaraka za makubaliano pamoja na Mkurugenzi wa Lindi Jumbo, Andrew Cunningham (wa tatu kulia), na Mwakilishi wa Gemcorp, William Binedell (wa pili kulia), wakati wa hafla rasmi ya utiaji saini wa makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Lindi Jumbo Limited kuhusu ushiriki wa Serikali katika Mradi wa kinywe wa kampuni hiyo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi. Kulia ni Mwanasheria na Katibu wa Kampuni ya Lindi Jumbo, Ephraim Mrawa.



Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde, akihutubia wakati wa hafla rasmi ya utiaji saini wa makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Lindi Jumbo Limited kuhusu ushiriki wa Serikali katika Mradi wa kinywe wa kampuni hiyo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi.
Mkurugenzi wa Lindi Jumbo, Andrew Cunningham, akitoa shukrani baada ya hafla ya utiaji saini wa makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Lindi Jumbo Limited kuhusu ushiriki wa Serikali katika Mradi wa Kinywe wa kampuni hiyo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi. Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde, alikuwa mgeni rasmi.


Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde (kushoto), akipokelewa na Mtendaji Mkuu wa Lindi Jumbo, Paul Lombar, kabla ya kuongoza hafla ya utiaji saini wa makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Lindi Jumbo Limited kuhusu ushiriki wa Serikali katika Mradi wa kinywe wa kampuni hiyo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi.


Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde (kushoto), akipokelewa na Mkurugenzi wa Lindi Jumbo, Andrew Cunningham, alipoenda kuwa mgeni rasmi katika hafla ya utiaji saini wa makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Lindi Jumbo Limited kuhusu ushiriki wa Serikali katika Mradi wa kinywe wa Lindi Jumbo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi. Wa pili kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea na Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mheshimiwa Mohamed Moyo.

Shirika la Mpango wa Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) Tanzania limesaini Hati za Makubaliano (MoUs) na taasisi 10 za elimu ya juu nchini kwa lengo la kuimarisha ajira kwa wahitimu, maendeleo ya ujuzi wa vitendo, ubunifu pamoja na kuwaandaa vijana kwa soko la ajira.

Makubaliano hayo yamesainiwa Mei 29, 2026 jijini Dar es Salaam ikiwa ni sehemu ya kuimarisha ushirikiano kati ya UNDP Tanzania na taasisi za elimu ya juu kupitia programu za wanafunzi, ubunifu, majadiliano ya kimkakati pamoja na ushirikishwaji wa taasisi mbalimbali.

Ushirikiano huo unatekelezwa kupitia Programu ya Maendeleo ya Vipaji kwa Vijana ya UNDP (UNDP Young Talent Development Programme), inayolenga kuunganisha vyuo vikuu, taasisi za maendeleo pamoja na sekta binafsi katika kusaidia mafunzo ya vitendo, ubunifu, ushauri wa kitaalamu na maandalizi ya ajira kwa wanafunzi na wahitimu vijana.

Akizungumza wakati wa hafla ya utiaji saini   makubaliano hayo, Mwakilishi Mkazi wa UNDP Tanzania,  Shigeki  Komatsubara  alisema ushirikiano huo unaonesha dhamira ya pamoja ya kuwaandaa vijana kwa dunia inayobadilika kwa kasi.

“Mpito kutoka chuoni kwenda katika maisha ya kazi haupaswi kuachiwa bahati nasibu. Vijana wanapaswa kuhitimu sio tu wakiwa na vyeti, bali pia wakiwa na uzoefu, uelewa na mwelekeo wa maisha yao ya baadaye,” alisema.

Kwa upande wake, Naibu Mkuu wa Chuo anayeshughulikia Taaluma, Utafiti na Ushauri wa Kitaalamu katika Taasisi ya Uhasibu Arusha (IAA), alisema ushirikiano huo ni hatua muhimu katika kuimarisha uhusiano kati ya vyuo vikuu na fursa kwa vijana.

“Vyuo vikuu vinaweza kutoa elimu ya darasani, lakini ushirikiano wa namna hii unasaidia kuwaunganisha wanafunzi na uzoefu wa vitendo, ushauri wa kitaalamu pamoja na fursa mbalimbali zinazowasaidia kujiandaa kwa maisha ya baadaye,” alisema.

Mpango huo unatarajiwa pia kuziwezesha taasisi za elimu ya juu kuwa sehemu muhimu katika kuchangia agenda ya maendeleo ya Tanzania kupitia ubunifu, tafiti, uongozi wa vijana na utoaji wa suluhisho kwa changamoto za maendeleo ya taifa.




 

TAASISI ya Afya na Tumaini Endelevu (ATE) imetoa elimu ya afya ya hedhi kwa wasichana wa Shule ya Msingi Uhuru Mchanganyiko ya jijini Dar es Salaam, pamoja na msaada wa pedi hizo ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya siku ya hedhi salama duniani.

Akizungumza katika tukio hilo lililoenda pamoja na utoaji wa msaada wa pedi hizo kwa kundi hilo la wasichana wenye mahitaji maalum, Mwenyekiti wa ATE, Bi. Lilian Lema amesema wametoa elimu ya afya ya hedhi kwa wasichana hao ili iweze kuwasaidia.

“Leo tunatoa elimu kuhusu hedhi salama, usafi wa mwili wa mwanamke, na tunagawa pedi pamoja na kuhamasisha jamii kuwalinda watoto kuanzia ngazi ya familia na vitendo vyote vya unyanyasaji wa kijinsia,” alisema Bi. Lema katika ziara hiyo.

Alisema wameguswa kusaidia kundi hilo la wasichana wenye mahitaji maalumu kwa sababu mara nyingi hukumbana na changamoto katika kupata taarifa sahihi, vifaa vya hedhi salama, na mazingira yanayowajali.

Taarifa zaidi zinabainisha baadhi ya wasichana hujikuta wakikosa masomo kwa siku tatu hadi saba kila mwezi wanapokuwa kwenye hedhi kwa sababu ya kukosa ‘pedi’.
Wasichana hao hulazimika kubaki nyumbani wakihofia kuchafuka na kuaibika mbele za watu, huku wakijikuta wakikosa fursa ya kushiriki masomo na wenzao kwa kipindi hicho.

Bi. Lema alifafanua zaidi kuwa, upatikanaji wa uhakika wa pedi kwa wanafunzi wa kike wakiwemo wa shule za msingi na sekondari nchini utaimarisha elimu ya mtoto wa kike kiujumla.

"Mtoto wa kike anapokuwa na uhakika wa kupata vifaa vya kujihifadhi anapokuwa katika siku zake inampa amani ya kujifunza na kuzingatia masomo yake bila ya kuwa na wasiwasi wa kuchafuka,"alisema.

Naye, Makamu Mkuu wa Shule ya Msingi Uhuru Mchanganyiko, Ajrath Kashakara amewaomba wadau anuai kuendelea kutoa elimu kuhusu masuala ya hedhi salama na umuhimu wa elimu ili kuendelea kubadilisha maisha ya wasichana na jamii ya kitanzania.







 

-Yasisitiza inathamini maisha ya mtu na utu wa mtu kwani wananchi wana haki yakuishi bila hofu

-Pia yazungumzia inavyotambua nafasi ya vijana na hatua inazochukua kuwapatia fursa



Na Said Mwishehe,Michuzi TV


CHAMA Cha Mapinduzi(CCM) kimesemakinathamini maisha ya mtu na utu wa mtu , kwahiyo mambo ya utekaji ambayo yapoyanafahamika kwenye jamii na ukwelihaifurahishwi na matukio hayo.

Akizungumza katika mahojiano maalum naCrown Media yaliyokuwa yakiongozwa naMtangazaji Salim Kikeke, Chama hichokupitia Katibu Mkuu wake Dk.Asha-Rose Migiro kimeeleza hatua kwa hatua kuhusu matukio hayo ya utekaji.

“Chama Cha Mapinduzi kinasema nchi hii wananchi wake wana haki ya kuishi bilahofu,kwahiyo hatuwezi kuunga mkonosuala la utekaji.Tunaguswa sanakwasababu katika huu utekaji wako pia wanachama wetu wameathirika ,kwahiyohatuwezi kutoguswa.Wapo wanachamaambao nao wameingia katika kadhia hiyolabda sio wengi lakini na sisi ndani yaChama Cha Mapinduzi tunalifahamu hilo.

“Lakini tunafahamu vyombo vya dola nahasa Polisi wamekuwa wakifanyauchunguzi na sisi tunataka hatua kama hizozichukuliwe ili nchi yetu tuishi kwa utulivuna bila hofu.

Kuhusu ripoti ya Jaji Chande kuoneshamoja ya vichocheo vya vurugu za Oktoba29 ni vijana kutokuwa na fursa, kutokuwana nafasi za ajira, Dk.Migiro amesemawanapozungumzia vijana wanazungumziatnguvu kazi ya taifa hili ,pia wanazungumziamustakabali wa nchi yetu.

“Kwasababu kwa hakika taifa la leo na la kesho ni la vijana .Kwa kuzingatia hiloChama Cha Mapinduzi kimekuwa makinikatika Ilani yake.Tumebainisha umuhimuwa nguvu kazi ya vijana , tumebainishahaja ya kuwekeza na kuwa na mikakatikatika sekta mbalimbali, kilimo, viwanda , biashara ,uvuvi ,masuala ya kidijitali nakujenga weledi na stadi za maisha kwambatuwekeze zaidi hapa kwasababu yakuwajenga vijana wa taifa letu tukitambuanguvu ya taifa letu inatokana na nguvu yavijana,”amesema Dk.Migiro.

Pia amesema licha ya kuweka kwenye Ilani ,Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 ambayoilisimamiwa na Serikali ya Chama Cha Mapinduzi imeweka wazi nafasi ya vijanana haja ya kuhakikisha wanachukua nafasiyao katika masuala yote ya kijamii, kiuchumi na kisiasa .”Kwahiyo vijana wanchi yetu hawajatelekezwa na Chama Cha Mapinduzi .

“Lakini mara baada ya Uchaguzi Mkuuwakati Rais anaunda Baraza la Mawazirialiunda wizara mahususi ya maendeleo yavijana na akaiweka chini ya ofisi yake ilijicho lakini liwe karibu kuhakikisha vijanaksauti yao inasikika katika mipango ya nchiyetu ,mchango wao unapatikana kwakutumia nguvu yao ,weledi wao nachangamoto zao zinatizamwa.

“Kuna mipango ya kuwawezesha kiuchumi,kuna mambo yamewekea mkakati ,eneo la mitaji na siku hizi vijana wanajiunga katikamakundi mbalimbali pamoja na uanzishwajiwa shughuli hasa za kiuchumi na kidijitali,hiyo yote ni mipango na sera za Chama Cha Mapinduzi. Hakuna namna CCM kitawaacha vijana wa nchi hii kwasababuhata takwimu za sensa zinaonesha vijanandio sehemu kubwa ya jamii yetu.”


Wafugaji nchini wameendelea kunufaika na huduma za kifedha baada ya kuongezeka kwa uelewa wao kuhusu masuala ya fedha na uwekezaji, hatua iliyowezesha kurahisishwa kwa vigezo vya dhamana ya kupata mikopo  kwa kutumia rasilimali walizonazo.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa Maonyesho ya Mifugo Kanda ya Ziwa, Meneja Biashara wa Benki ya CRDB Kanda ya Magharibi, Anselem Mwenda, amesema benki hiyo imefanikiwa kuwasaidia wafugaji wengi kupata mikopo kwa urahisi kupitia huduma mbalimbali ikiwemo bima ya mifugo.

Mwenda alitoa kauli hiyo mara baada ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Agnes Meena, kutembelea banda la CRDB, ambao ni wadhamini wakuu wa maonyesho hayo.

Alisema kuwa kwa sasa wafugaji wana uwezo wa kukopesheka kwa urahisi zaidi kutokana na kuwa na bima ya mifugo pamoja na kutambuliwa kwa rasilimali zao kama sehemu ya dhamana.

“Uelewa wa wafugaji umeongezeka kwa kiwango kikubwa tofauti na ilivyokuwa zamani. Hii imewasaidia kutumia fursa za kifedha zinazotolewa na benki kwa maendeleo ya shughuli zao."

Aliongeza kuwa huduma zote za kibenki zinaendelea kutolewa katika banda la CRDB kwa kipindi cha siku mbili za maonyesho hayo, kuanzia Mei 30 hadi 31, huku akiwakaribisha wafugaji na wadau wengine kufika kupata huduma pamoja na elimu ya masuala ya fedha.

Mwenda alisisitiza umuhimu wa wafugaji kuendelea kujifunza kuhusu usimamizi wa fedha na matumizi sahihi ya mikopo ili kuongeza tija katika sekta ya mifugo na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.



 

Wafugaji nchini wametakiwa kuachana na mbinu za jadi za ufugaji ambazo zimepitwa na wakati na badala yake kutumia teknolojia za kisasa za kidigitali zinazorahisisha usimamizi na ufuatiliaji wa mifugo kuanzia inapozaliwa hadi hatua ya kuchinjwa.

Wito huo umetolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Climb Up Limited, Emmanuel Ngallah, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika Maonyesho ya Mifugo Kanda ya Ziwa Mei 30, 2026, mkoani Shinyanga.

Ngallah alisema matumizi ya mifumo ya kidigitali katika sekta ya mifugo yanawawezesha wafugaji kupata taarifa sahihi kuhusu afya, ukuaji na historia ya mifugo yao, jambo linaloongeza tija na thamani ya biashara ya mifugo.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Agnes Meena mgeni rasmi katika maonyesho hayo, alisisitiza umuhimu wa wafugaji kuendana na mabadiliko ya teknolojia ili kuongeza uzalishaji na kuifanya sekta ya mifugo kuwa na mchango mkubwa zaidi katika uchumi wa nchi.

Alieleza kuwa serikali inaendelea kuhamasisha matumizi ya teknolojia katika ufugaji ili kuboresha usimamizi wa mifugo, kuongeza ubora wa bidhaa zinazotokana na mifugo na kufungua fursa zaidi za masoko ya ndani na nje ya nchi.

Wakati huo huo, baadhi ya wananchi waliotembelea banda la Climb Up Limited katika maonesho hayo wameeleza kufurahishwa na elimu waliyoipata kuhusu ufugaji wa kisasa na matumizi ya mifumo ya kidigitali.

Wamesema maarifa hayo yatawasaidia kuboresha shughuli zao za ufugaji, kuongeza uzalishaji na kufuatilia kwa urahisi maendeleo ya mifugo yao kwa kutumia teknolojia.

Maonesho ya Mifugo Kanda ya Ziwa yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kuwakutanisha wadau wa sekta ya mifugo, kampuni za teknolojia na wafugaji kwa lengo la kubadilishana uzoefu na kuhamasisha matumizi ya mbinu za kisasa katika uzalishaji wa mifugo.





 


Top News