Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Ngwaru Jumanne Maghembe (Mb.), ameshiriki Mhadhara maalum wa kuadhimisha Miaka 51 ya Uhuru wa Muungano wa Visiwa vya Comoro uliofanyika katika Kituo cha Uhusiano wa Kimataifa cha Dkt. Salim Ahmed Salim, jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika mhadhara huo, Mhe. Dkt. Maghembe amesisitiza dhamira ya Tanzania kuimarisha uhusiano wa kihistoria na ushirikiano wa karibu na Jamhuri ya Muungano wa Visiwa vya Comoro. 

Ameipongeza Serikali na wananchi wa Comoro na kumshukuru Balozi wa Visiwa vya Comoro nchini Mhe. Dr. Ahamada El Badaoui Mohamed Fakih kwa kuandaa tukio hilo muhimu. Aidha, amekumbusha mchango wa Tanzania chini ya uongozi wa Hayati Julius Kambarage Nyerere katika kusaidia harakati za uhuru wa Comoro.

Naye Balozi wa Visiwa vya Comoro Mhe. Fakih aliishukuru Serikali ya Tanzania kwa mchango wake mkubwa katika harakati za ukombozi zilizopelekea Uhuru wa Comoro mwaka 1975. 

Alisisitiza kuwa Tanzania imeendelea kuwa mshirika muhimu katika kuimarisha amani, maendeleo na ushirikiano wa kikanda. Nchi hizo mbili zinaendelea kushirikiana kwa karibu katika sekta mbalimbali zikiwemo afya, ulinzi na usalama, biashara na uwekezaji, uchukuzi, bandari na elimu kwa manufaa ya wananchi wa pande zote mbili.


















 



Dar es Salaam

Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) limeendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu mchango wa sayansi ya visukuku mimea (Palynology) katika utafiti wa mafuta na gesi asilia kupitia Banda la TPDC kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa (Sabasaba).

Mtafiti Mwandamizi wa Visukuku Mimea wa TPDC, Bw. Johanes Kakoki, alisema uchambuzi wa visukuku mimea kama dinoflagellates ( viumbe vidogo sana vya majini aina ya planktoni) , chavua (pollen) na mbeguchembe (spores) husaidia kubaini umri wa miamba na uwezo wake wa kuzalisha na kuhifadhi mafuta au gesi asilia.

Aliongeza kuwa taarifa hizo huunganishwa na tafiti za kijiolojia, kijiofizikia na kijiokemia ili kuongeza usahihi wa kubaini maeneo yenye rasilimali za mafuta na gesi, huku teknolojia za kisasa zikiboresha ufanisi wa tafiti na kupunguza gharama.

Kupitia maonesho hayo, TPDC inaendelea kuelimisha wananchi kuhusu hatua za utafiti wa mafuta na gesi asilia na mchango wa tafiti za kisayansi katika maendeleo ya sekta na uchumi wa Taifa.

#Tunaboreshamaishanakuwezeshamaendeleo


Na Mwandishi Wetu

IRINGA – Mbunge wa Jimbo la Ismani, Mhe. Emmanuela Mtatifikolo, amezindua rasmi maonesho na sherehe za Sabasaba zinazofanyika katika Kata ya Ilolo Mpya, Tarafa ya Pawaga, wilayani Ismani, huku akiwataka wananchi kutumia maonesho hayo kujifunza, kufanya biashara na kuimarisha mshikamano wa kijamii.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mhe. Mtatifikolo alisema maonesho ya Sabasaba ni fursa muhimu kwa wananchi kukutana, kubadilishana uzoefu, kuuza na kununua bidhaa mbalimbali pamoja na kujifunza fursa za maendeleo kutoka kwa washiriki na wageni wanaotoka maeneo mbalimbali nchini.


Aliwahamasisha wananchi wa Kata ya Ilolo Mpya na Jimbo la Ismani kwa ujumla kushiriki kikamilifu katika shughuli hizo, akieleza kuwa mbali na burudani, maonesho hayo yana mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa wananchi na kuimarisha mahusiano ya kijamii.

"Mnatakiwa kutumia maonesho haya kama jukwaa la kujifunza, kufanya biashara na kujenga mahusiano yatakayochochea maendeleo ya Ismani na wananchi wake," alisema Mtatifikolo.

Mbunge huyo pia aliwataka vijana kuendelea kufanya kazi kwa bidii na kujiepusha na vitendo vinavyoweza kuhatarisha amani na utulivu wa nchi, akisisitiza kuwa maendeleo hayawezi kupatikana bila kuwepo kwa mazingira ya amani.



Aidha, aliwahimiza wazazi na walezi kuendelea kuwalea watoto katika misingi ya maadili, uzalendo na uwajibikaji ili kujenga kizazi kitakachochangia maendeleo ya taifa.

"Malezi bora ndiyo msingi wa kujenga taifa lenye vijana wenye nidhamu, uzalendo na uwezo wa kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya nchi," alisisitiza.

Maonesho hayo ya Sabasaba yanajumuisha shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi, zikiwemo maonesho ya bidhaa, michezo ya mpira wa miguu, ngoma za asili pamoja na burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali.



Waandaaji wa maonesho hayo wamesema lengo ni kutoa fursa kwa wananchi kuonesha bidhaa na huduma zao, kuhamasisha biashara ndogondogo na kukuza vipaji vya vijana kupitia michezo na sanaa.

Sherehe hizo hufanyika kila mwaka baada ya wananchi kumaliza shughuli za uvunaji, zikiwa sehemu ya kuimarisha mshikamano wa jamii, kuchochea biashara na kutoa burudani kwa wakazi wa Ismani na maeneo jirani.

Wananchi waliohudhuria uzinduzi huo walieleza kufurahishwa na maandalizi ya maonesho hayo, wakisema yameendelea kuwa kichocheo cha maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika Jimbo la Ismani.
SPIKA wa Bunge, Mussa Zungu, amesema hakuna Bunge gumu, kali, bovu wala dhaifu, akisisitiza kuwa jukumu la Bunge ni moja tu, kuhakikisha ustawi wa wananchi katika nyanja mbalimbali za maendeleo.

Zungu alieleza hayo akijibu maswali ya baadhi ya wahariri wa vyombo vya habari katika mkutano wake na wahariri hao kuhusu maadhimisho ya miaka 100 ya Chimbuko la Bunge uliofanyika jana Dar es Salaam. Akijibu swali kuhusu mtazamo kuwa Bunge la sasa ni dhaifu kutokana na uwepo wa idadi ndogo ya wabunge wa upinzani, alisema mtazamo huo si wa kweli.

Alisema hakuna Bunge lililokuwa bovu, kali au dhaifu, kwani mabunge yote yana jukumu moja la kusimamia ustawi wa jamii kupitia sekta mbalimbali ikiwemo mazingira, afya, elimu na makazi ya wananchi.

“Naomba niseme kitu tena hili mchukue maelezo, hakuna Bunge dhaifu, hatupigani, Bunge siyo klabu ya mapambano, bungeni tunakaa, tunajenga hoja na tunajibu hoja kwa hoja,” alisema.

Alisema si sahihi kulitaja Bunge kuwa dhaifu kwa sababu halijaitaka Serikali kuondoa kodi ya bodaboda au kodi ya kilimo, akieleza kuwa Bunge limekuwa likitoa maelekezo kwa Serikali kuhusu masuala mbalimbali ikiwemo sera za kodi na matumizi ya magari ya gharama kubwa.

Aliongeza kuwa mawaziri husimama Bungeni kueleza msimamo wa Serikali, lakini pale ambapo Bunge halikubaliani na Serikali, hutoa maelekezo kwa kuwa ni mhimili wa dola wenye jukumu la kuisimamia Serikali.

Kuhusu hoja ya Bunge kukosa mvuto kutokana na idadi ndogo ya wabunge wa upinzani, Zungu alisema katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 vyama vya upinzani vilipata jumla ya wabunge 102 chini ya Katiba na Tume ileile ya Uchaguzi, na kambi rasmi ya upinzani iliundwa baada ya kufikia idadi iliyohitajika.

“Mtakumbuka mwaka 2015 upinzani ulikuwa na nguvu kubwa ndani ya Bunge. Dar es Salaam kulikuwa na majimbo mengi ya upinzani ikiwemo Kinondoni, Ubungo na Kigamboni. Hata katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa walishinda maeneo mengi,” alisema.

Alisema wananchi waliwapa nafasi ya kuongoza katika maeneo mbalimbali, lakini hali ya sasa ya kuwa na wabunge wachache wa upinzani ni matokeo ya maamuzi ya wananchi kupitia uchaguzi. “Kwa uongozi wa vyama vya siasa wa sasa wanaviongozi wazuri lakini bado hawajawa na hamasa ya kuwashawishi wananchi vya kutisha ili kuwachagua,” alisema Zungu.

Awali, akizungumzia maadhimisho ya miaka 100 ya Chimbuko la Bunge, Zungu alisema Bunge limepitia mabadiliko mbalimbali ya kanuni yaliyosaidia kuimarisha demokrasia, maendeleo ya taifa na ushiriki wa wananchi katika uongozi. Alisema ushiriki wa wanawake umefikia asilimia 40, huku idadi ya wabunge vijana ikifikia 72 na wabunge wenye ulemavu kufikia 11, hatua aliyoeleza kuwa inaonesha mafanikio ya maboresho yaliyofanyika katika kipindi cha miaka 100 ya Bunge.




Na Karama Kenyunko Michuzi Tv
WAZIRI wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda ameitaka Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) kujitathmini kwa uhalisia wanapokwenda kuadhimisha miaka 40 badala ya kujikita zaidi katika kusherehekea mafanikio.

Profesa Mkenda ametoa wito wa tafakuri hiyo leo Julai 2, 2026 jijini Dar es salaam wakati wa uzunduzi wa miaka 40 ya COSTECH (COSTECH@40) pamoja na Mfumo wa Taifa wa Taarifa za Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (National Information System for Science, Technology and Innovation – NISSTI).

Akizungumza wakati wa uzunduzi huo, amesema tathmini ya miaka 40 ya Costech inapaswa kuwa ya kina na yenye kuangalia mchango halisi wa sayansi katika maisha ya watanzania, akisisitiza sayansi na ubunifu vinapaswa kupimwa kwa matokeo yaliyo wazi na sip kwa sherehe au taswira za nje.

Utafiti unahitaji uhuru wa kitaaluma, lakini mafanikio yake yanategemea uratibu madhubuti, ushirikiano wa sekta zote na mfumo wa kitaifa unaounganisha juhudi za taasisi mbalimbali kwa maendeleo ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu." Amesems Prof. Mkenda

"Sera yetu mpya lazima iendane na mahitaji ya wakati na iwe chachu ya mageuzi. Tuwe na ndoto kubwa, tufikiri picha pana na tuthubutu kuchukua hatua, kwa sababu bahati huwapendelea wanaothubutu.

Aidha ametoa wito kwa watafiti, taasisi za utafiti, wavumbuzi na wadau wote kujisajili kwenye Mfumo wa Kitaifa wa Taarifa za Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (NISSTI) na kuhakikisha taarifa zao zinahuishwa mara kwa mara na kwamba Mafanikio ya mfumo huo yanategemea ushiriki wa kila mmoja."

"Nawaalika vijana wa Tanzania kuikumbatia Sayansi, Teknolojia na Ubunifu kama njia ya kutatua changamoto za jamii, kuunda ajira na kuijenga Tanzania yenye uchumi shindani unaotegemea maarifa, ubunifu na teknolojia. Mustakabali wa Taifa letu uko mikononi mwa vijana wake."

Amesisitiza sayansi na teknolojia lazima zielekezwe kuongeza tija na mavuno kwa wakulima ili Tanzania iweze kushindana katika masoko ya kimataifa na kuinua uchumi wa wananchi wake, hivyo matokeo ya utafiti yanapaswa kuonekana sokoni na si kaulimbiu au maonesho ya muda.

Pia alisisitiza taasisi za utafiti kuchunguza kisayansi tiba za asili kwa kufanya majaribio ya awali na ya kitabibu ili kuthibitisha uhalisia wake ili kama zinafanya kazi zigeuzwe kuwa bidhaa rasmi za dawa na kama hazifanyi kazi basi wananchi waelezwe.
Katibu Mkuu Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia Profesa Caroline Nombo alisema wanapoadhimisha miaka 40 wanapata nafasi ya kutafakari historia ya uwekezaji wa Serikali katika sayansi, teknolojia na ubunifu pamoja na mchango wake katika kutatua changamoto za jamii.

"Kipaumbele chetu ni kuhakikisha maarifa yanayozalishwa katika vyuo vikuu, taasisi za utafiti, maabara, vituo vya ubunifu na sekta binafsi yanachangia maendeleo ya sekta za kipaumbele za taifa." Amesema.
Akizungumzia kuhusu mfumo wa NISST Mkurugenzi Mkuu wa Costech, Dkt. Amos Nungu amesema maadhimisho ya COSTECH@40 si ya kuangalia tulikotoka pekee, bali ni ya kujenga Tanzania tunayoitaka kupitia Sayansi, Teknolojia na Ubunifu kuelekea Dira ya Taifa 2050."

"Sayansi na ubunifu lazima vionekane, vieleweke, vifikike kwa urahisi na viwe na manufaa ya moja kwa moja kwa wananchi." Amesema Prof. Nungu.

Amesema, mustakabali wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu nchini utajengwa kwa ushirikiano, maarifa ya pamoja na ushiriki wa wadau wote hivyo tunataka kila mtafiti, mbunifu na taasisi ionekane, iunganishwe na ipate fursa kupitia mfumo mmoja wa kitaifa."

"Miaka 40 ya COSTECH ni urithi wa mafanikio; miaka 40 ijayo lazima iwe safari ya matokeo makubwa zaidi kwa maendeleo ya taifa.... Ushindani wa Tanzania katika uchumi wa maarifa utaimarishwa kwa kuwekeza katika Sayansi, Teknolojia na Ubunifu." amesema Dkt Nungu.

Naye John Kondoro, Mwenyekiti wa Kamisheni ya Costech amesema, Costech taendelea kuisimamia Tume kwa karibu ili kuhakikisha maelekezo ya Serikali yanatekelezwa kwa weledi, kwa wakati na kwa matokeo yanayopimika."

"Taarifa zinazopatikana kupitia NISSTI zinapaswa kuwa msingi wa kupanga vipaumbele vya taifa, kuelekeza uwekezaji na kuongeza tija ya utafiti na ubunifu".


Serikali ya Mkoa wa Dodoma imewataka wafanyabiashara, wawekezaji, washauri wa kodi na wananchi kuendelea kushirikiana na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwa kuzingatia sheria za kodi ili kuongeza mapato ya Serikali na kuchochea maendeleo ya Taifa.

Wito huo umetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Chamwino, Mhe. Janeth Mayanja, aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Dodoma katika maadhimisho ya miaka 30 ya TRA na hafla ya utoaji wa Tuzo za Mheshimiwa Rais kwa Walipakodi Bora,Julai 1, 2026 Jijini Dodoma.

Mhe. Mayanja amesema wafanyabiashara wanapaswa kusajili biashara zao kwa mujibu wa sheria, kutunza kumbukumbu sahihi za biashara, kuwasilisha ritani za kodi kwa wakati na kulipa kodi kwa hiari, kwa wakati na kwa usahihi.

Aidha, amewahimiza kutumia mifumo rasmi ya Serikali katika kufanya malipo, kutumia mashine za EFD ipasavyo na kutoa risiti halali kwa kila mauzo, huku akiwataka wananchi kudai risiti kila wanaponunua bidhaa au huduma na kuepuka vitendo vya ukwepaji wa kodi vinavyokwamisha maendeleo ya Taifa.

Amesema ushirikiano huo utawezesha Serikali kuongeza mapato na kutekeleza miradi mingi zaidi ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi, huku Mkoa wa Dodoma ukiendelea kushirikiana kwa karibu na TRA kuhakikisha mazingira ya biashara yanakuwa rafiki na changamoto za walipakodi zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati.

Kwa upande wake, Kaimu Meneja wa TRA Mkoa wa Dodoma, John Njau, amesema maadhimisho ya miaka 30 ya TRA ni fursa ya kutafakari mafanikio yaliyopatikana tangu kuanzishwa kwa mamlaka hiyo mwaka 1996, ikiwemo maboresho ya mifumo ya ukusanyaji wa mapato, matumizi ya teknolojia za kidijitali na utoaji wa huduma bora kwa walipakodi.

Njau amesema mafanikio hayo yamechangiwa na ushirikiano wa walipakodi na wadau mbalimbali, huku akiwapongeza walipakodi wanaotekeleza wajibu wao kwa hiari na waliotunukiwa Tuzo za Rais kwa Walipakodi Bora kwa kuwa mfano wa kuigwa katika kujenga uchumi wa Taifa.

Naye Mwenyekiti wa Washauri wa Kodi Mkoa wa Dodoma, CPA Dkt. Lucas Webie, amewataka wafanyabiashara kuacha kuiangalia TRA kama adui, akisema mamlaka hiyo hutoa nafasi ya kusikiliza changamoto za walipakodi na kuweka utaratibu wa ulipaji wa kodi kwa awamu, huku akisisitiza kuwa mapato ya kodi ndiyo msingi wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo nchini.








▪️ Waziri Mavunde akutana na mwekezaji wa kiwanda cha kuzalisha goroli za chuma

▪️ Kiwanda hicho kinatarajiwa kujengwa Buzwagi Special Economic Zone, Kahama

▪️ Oriental Casting and Forging Ltd ya China yajipanga kuwekeza nchini

▪️ Serikali yalenga kupunguza utegemezi wa bidhaa za migodini kutoka nje

▪️ Tanzania yajipanga kuwa kitovu cha uzalishaji na usambazaji wa bidhaa za migodini Afrika

Dar es Salaam: Tanzania imeanza kujipanga kuwa kitovu cha uzalishaji na usambazaji wa bidhaa za migodini barani Afrika, baada ya Serikali kuvutia uwekezaji wa viwanda vitakavyozalisha bidhaa muhimu zinazotumiwa na wachimbaji wakubwa na wadogo nchini.

Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, leo amekutana na Mkurugenzi Mkuu na mmiliki wa kampuni ya Oriental Casting and Forging Ltd ya China, Hou Songcun, kujadiliana kuhusu uwekezaji wa kiwanda cha kuzalisha goroli za chuma zinazotumika kusaga miamba ya madini katika shughuli za uchenjuaji.

Mavunde amewakaribisha wawekezaji hao kujenga kiwanda hicho katika eneo la Buzwagi Special Economic Zone lililopo Kahama, Shinyanga, ambalo Serikali imelitenga kwa ajili ya uwekezaji wa viwanda vinavyohudumia Sekta ya Madini.
Amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeweka mazingira mazuri ya uwekezaji na sasa inalenga kuvutia viwanda vitakavyozalisha bidhaa za migodini ndani ya nchi, badala ya kuendelea kutegemea uagizaji kutoka nje.

“Lengo letu ni kuona wachimbaji wakubwa na wadogo hapa nchini wanapata bidhaa nyingi za kuzalisha madini bila kutegemea sana uagizaji wa bidhaa hizo kutoka nje ya nchi,” amesema Mavunde.

Amesema Tanzania ina nafasi kubwa ya kuwa kitovu cha uzalishaji na usambazaji wa bidhaa za migodini barani Afrika kutokana na ukuaji wa Sekta ya Madini, mahitaji makubwa ya bidhaa hizo na mazingira bora ya uwekezaji yaliyowekwa na Serikali.

Kwa mujibu wa Mavunde, uwekezaji wa viwanda vinavyohudumia Sekta ya Madini utaongeza ajira, kupunguza gharama za uzalishaji kwa wachimbaji, kuimarisha mnyororo wa thamani wa madini na kuongeza ushiriki wa viwanda vya ndani kwenye uchumi wa madini.
Amesema Serikali itaendelea kuvutia na kuunga mkono wawekezaji wanaolenga kujenga viwanda vinavyounganisha uchimbaji wa madini na uzalishaji wa bidhaa zinazotumika migodini, ili kuongeza manufaa ya sekta hiyo kwa uchumi wa Taifa.

Kwa upande wake, Hou Songcun amesema kampuni yake iko tayari kufanya uwekezaji mkubwa nchini kwa kuwa Tanzania ina mazingira rafiki ya uwekezaji na Sekta ya Madini inaendelea kukua kwa kasi.

Amesema uzalishaji wa bidhaa za migodini ndani ya Tanzania utarahisisha upatikanaji wa vifaa hivyo kwa wachimbaji, kupunguza utegemezi wa bidhaa zinazoagizwa kutoka nje ya nchi na kuongeza uhakika wa upatikanaji wa bidhaa muhimu katika shughuli za uchimbaji.

Kiwanda hicho kinatarajiwa kuongeza uwezo wa Tanzania kuzalisha bidhaa muhimu za migodini ndani ya nchi, kuimarisha viwanda vinavyohudumia Sekta ya Madini na kuiweka Kahama katika nafasi muhimu ya uzalishaji wa bidhaa za migodini kwa soko la ndani na la kikanda.

-Watuhumiwa 188 washikiliwa wakuhusishwa na dawa hizo,sheria kuchukua mkondo wake


Na Said Mwishehe,Michuzi TV

MAMLAKA ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imefanya operesheni maeneo mbalimbali nchini na kufanikiwa kukamata tani 22.6 za dawa za kulevya, lita 30.5 na kilogramu 19.94 za dawa tiba zenye asili ya kulevya. 

Pia, imeteketeza ekari 228.5 za mashamba ya bangi pamoja na tani 3.3 za bangi na mirungi huku ikiyashikilia magari sita, bajaji mbili na pikipiki 33 zilikamatwa kuhusiana na uhalifu huo wakati watuhumiwa 188 wamekamatwa kwa hatua za kisheria.

Akizungumza jijini Dar es Salaam leo Julai 2,2026 Kamishina Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Aretas Lyimo amesema operesheni hiyo imefanyika kati ya Mei na Juni mwaka huu.

Amesema operesheni zilizofanyika Dar es Salaam zilifanikisha ukamataji wa kilogramu 19.94 za bidhaa zilizotambulishwa kama virutubisho vya lishe aina ya AFA CELL (Moringa Extract) katika eneo la mizigo inayosafirishwa kwenda nje ya nchi kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere. 

“Baada ya kufanyiwa uchunguzi wa maabara, ilibainika kuwa bidhaa hizo zilikuwa na kiambata cha dawa tiba yenye asili ya kulevya aina ya Prazepam. Bidhaa hizo ziliingizwa nchini kutoka Malaysia na zilikuwa zinaandaliwa kusafirishwa kwenda Barbados katika visiwa vya Karibiani. 

Amefafanua katika tukio hilo watuhumiwa Agustino Metusela Ismaely (30), mkazi wa Kimara; Zamia Harid Upunda (23), mkazi wa Bungoni, Ilala; na Habiba Ally Mziga (54), mkazi wa Mbezi Makonde walikamatwa.

“Prazepam ni dawa tiba yenye asili ya kulevya iliyopo katika kundi la benzodiazepine inayotumika kutibu magonjwa mbalimbali ikiwemo wasiwasi, msongo wa mawazo na kukosa usingizi. Endapo dawa hizi zitatumika kiholela au bila maelekezo ya daktari zinaweza kusababisha uraibu, kuharibu mfumo wa fahamu, mfumo wa upumuaji, kupoteza fahamu na hata kifo.”

Katika operesheni nyingine iliyofanyika mtaa wa Manyanya, Kinondoni, amesema zilikamatwa kilogramu 34.87 za mirungi iliyokuwa ikisafirishwa kwa kutumia gari aina ya Fuso lenye namba za usajili T 490 ECM kutoka Tarakea, mkoa wa Kilimanjaro. 

Amesema Mirungi hiyo iliyotokea nchini Kenya ilikuwa imefichwa kwa kuchanganywa na matenga ya nyanya ili kuficha uhalisia wa mzigo huo. Baada ya kufikishwa Dar es Salaam, ilishushwa katika eneo la kituo cha mafuta kilichopo mtaa huo kabla ya kuanza kusambazwa kwa kutumia usafiri wa bajaji yenye namba za usajili MC 361 CZV.

“Katika tukio hilo, walikamatawa watuhumiwa Mohamed Omary Mohamed (24), utingo na mkazi wa Tandale; Suleman Omary Suguti (34), dereva wa gari hilo na mkazi wa Tarakea, Rombo; na Deo Paschal Maratua (32), dereva wa bajaji na mkazi wa Tandale kwa Mtogole. 

“Mtuhumiwa Husseni Jumaa

Salimu (52), mkazi wa Dar es Salaam, ambaye anadaiwa kuwepo Nairobi, Kenya, anatafutwa kuhusiana na tukio hilo.”

Aidha amesema katika operesheni iliyofanyika eneo la ukaguzi wa mizigo la Bandari ndogo ya boti zinazotoa huduma kati ya Dar es Salaam na Zanzibar, zilikamatwa gramu 972.05 za mirungi zilizokuwa zikisafirishwa na mtuhumiwa Kalsam Abdurahman Sebbi (43), raia wa Kenya mwenye makazi yake Mombasa. 

Wakati wilayani Kigamboni mkoani Dar es Salaam  zilikamatwa gramu 162.48 za heroin zilizomuhusisha mtuhumiwa Omary Miraji Mbonaeni.

Pia mkoani Arusha, zilikamatwa kilogramu 106.04 za dawa za kulevya aina ya mirungi zilizokuwa zikisafirishwa kwa kutumia gari aina ya Toyota Premio lenye namba za usajili T 853 ECX. 

Kamishina Jenerali Lyimo amesema katika tukio hilo, alikamatwa mtuhumiwa Goodluck Erasto Nyakaselula (35), mkazi wa Mbezi Beach, Dar es Salaam, ambaye ni mtaalam wa picha za kitabibu (Radiographer) katika Hospitali ya Ocean Road ya jijini Dar es Salaam.

Aidha, wilayani Same mkoani Kilimanjaro, eneo la kituo cha mabasi yaendayo mikoani, zilikamatwa kilogramu 240 za mirungi zikiwa zimefichwa ndani ya mabegi ya nguo. Katika tukio hilo, walikamatwa watuhumiwa Irene Obedi Sule na Eliasi Obedi Sule.

Kufuatia operesheni zilizofanyika katika mikoa mingine nchini, zilikamatwa tani 19.5 za bangi, tani 2.6 za mirungi, gramu 11.63 za heroin na kilogramu 40 za skanka. 

Aidha, tani 3.3 za bangi na mirungi pamoja na ekari 228.5 za mashamba ya bangi ziliteketezwa katika wilaya za Chamwino mkoa wa Dodoma, kijiji cha Mwengei kilichopo wilaya ya Kilwa mkoa wa Lindi na katika vijiji vya Busekeseke na Miembeni vilivyopo wilaya ya Sengerema na Geita.




Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga (Mb), akipokelewa na Mkuu wa Mtandao wa Matawi na Mauzo wa Benki ya NMB, Donatus Richard, alipotembelea banda la benki hiyo katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam yanayoendelea katika Viwanja vya Saba Saba. 

Katika ziara hiyo, Waziri Kapinga alipewa maelezo kuhusu suluhisho mbalimbali za kibenki zinazochochea ukuaji wa biashara, ujumuishaji wa kifedha na mageuzi ya uchumi wa kidijitali nchini.







Top News