Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Alhaj Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amewahimiza waumini wa dini ya Kiislamu kuitumia vema misikiti kwa ajili ya kujadiliana na kuzipatia ufumbuzi changamoto zilizopo katika jamii.

Alhaj. Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 24 Aprili 2026, alipojumuika na waumini wa dini ya Kiislamu katika Sala ya Ijumaa iliyoambatana na ufunguzi wa Msikiti Mpya wa Jamaa Nour uliopo Boshowa, Nungwi, Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Ameeleza kuwa zipo changamoto nyingi katika jamii zinazohitaji kupatiwa ufumbuzi, hususan zile wanazokabiliana nazo watu wa makundi maalumu, wakiwemo wajane, wazee wasiojiweza, watoto, watu wenye ulemavu na mayatima.

Aidha, Alhaj Dkt. Mwinyi amesema waumini wana wajibu mkubwa wa kuitumia misikiti kusomesha dini, hususan kwa watoto ili waijue vema dini yao, pamoja na kusali kwa bidii na kumcha Mwenyezi Mungu, kwani hiyo ndiyo sababu kuu ya kujengwa misikiti mikubwa na mizuri katika maeneo mbalimbali.

Vilevile, Alhaj Dkt. Mwinyi amewahimiza waumini kuutunza msikiti huo mpya ili ubaki katika haiba na mazingira bora wakati wote, kwa kuweka utaratibu mzuri wa kuchangia, pamoja na kuwatunza maimamu na walimu wa madrasa, na kumshukuru mfadhili wa msikiti huo kwa uamuzi wake.









Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC) leo imezindua rasmi Kampeni ya “Linda Ushirika, Chagua Uadilifu”, ikiwa ni hatua muhimu katika kuhamasisha usimamizi bora na uadilifu katika sekta ya ushirika nchini. Kampeni hii inalenga kuelimisha na kuhamasisha Wanaushirika na wadau mbalimbali kuhusu umuhimu wa ushirika wenye uadilifu, uwazi, na ufanisi katika kuleta maendeleo endelevu.

Uzinduzi wa kampeni hiyo umefanyika jijini Dodoma, ambapo Waziri wa Kilimo, Mhe. Daniel Chongolo, alikuwemo kama mgeni rasmi kwenye Mkutano wa Wadau wa Maendeleo ya Ushirika. Katika hotuba yake, Chongolo alisisitiza kuwa ushirika ni nguzo muhimu katika uchumi wa Taifa, akiongeza kuwa ushirika wa kiuchumi na kijamii unaweza kutoa suluhu kwa changamoto kubwa zinazokumba sekta ya kilimo na uchumi wa nchi.

"Leo tunazindua kampeni hii kwa lengo la kuweka misingi imara ya ushirika. Ushirika unahitaji uadilifu, uwazi, na usimamizi bora ili uweze kutoa matokeo chanya kwa Wanaushirika na jamii kwa ujumla," alisema Mhe. Chongolo. Aliendelea kusema kuwa sekta ya ushirika ina mchango mkubwa katika uchumi wa Tanzania na kwamba juhudi zote za kuimarisha ushirika ni muhimu katika kuhakikisha nchi inapata maendeleo ya kudumu.

Amesema kuwa, ili sekta ya ushirika iweze kuleta matokeo bora, kila mdau katika sekta hiyo anahitaji kujitolea kwa dhati katika kusimamia rasilimali za ushirika, kwa kuzingatia misingi ya uadilifu na uwazi. "Tunahitaji kuwekeza katika mafunzo, uongozi bora, na kuhakikisha kuwa vyombo vya ushirika vinakuwa na uwezo wa kuongoza na kusimamia kwa ufanisi rasilimali zao," alisema Waziri Chongolo.

Chongolo pia amesisitiza kuwa serikali itaendelea kutoa msaada kwa sekta ya ushirika, ikiwa ni pamoja na kuboresha sera, mikopo, na mifumo ya usimamizi wa mali za ushirika. "Tunapokuwa na ushirika imara, tutakuwa na uchumi imara. Na kwa kufanya kazi pamoja, tunaweza kufikia malengo yetu ya maendeleo endelevu na kuwa na taifa lenye ustawi wa kiuchumi," alieleza.

Kwa upande wake, Dkt. Benson Ndiege, Mrajis na Mtendaji Mkuu wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika, amewahimiza Wanaushirika kuwa na ushirika imara na wenye uadilifu ili kuweza kuchangia kwa ufanisi katika uchumi wa Tanzania. Alieleza kuwa ushirika imara ni msingi wa ustawi wa kiuchumi na kijamii katika taifa letu.

Uzinduzi huo umehudhuriwa na wadau mbalimbali kutoka sekta ya ushirika, ikiwa ni pamoja na taasisi za kifedha, vyama vikuu vya ushirika, wakaguzi wa nje, wizara za serikali, na mashirika ya kimataifa, ambao wamejizatiti kutoa mchango wao katika kuimarisha sekta ya ushirika na kuboresha hali ya maisha ya Wanaushirika.

Kampeni ya “Linda Ushirika, Chagua Uadilifu” ni mwendelezo wa jitihada za TCDC katika kuboresha ufanisi wa ushirika na kuhimiza utawala bora. TCDC inajivunia kufanya kazi kwa karibu na serikali, vyama vya ushirika, na wadau wengine muhimu katika sekta hii kwa lengo la kuleta mabadiliko ya kiuchumi na kijamii. Kampeni hii pia itahusisha semina, mafunzo, na mikutano ya kujenga uwezo kwa Wanaushirika kote nchini, ili kuhakikisha kuwa ushirika unakuwa na mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa Taifa.








Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, amewataka wanafunzi wa Shule ya Sekondari Mnazi Mmoja kusoma kwa bidii na kuzingatia masomo yao ili kuongeza kiwango cha ufaulu shuleni hapo.

Mpogolo ametoa kauli hiyo leo Aprili 24, 2026, wakati alipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa madarasa 20  na  matundu 45  ya vyoo  shule hapo, mradi unaotekelezwa kwa gharama ya sh. bilioni 1.8.

Amesema kukamilika kwa mradi huo kutasaidia kupunguza changamoto ya uhaba wa vyumba vya madarasa iliyokuwepo kwa muda mrefu na kuwawezesha wanafunzi kusoma katika mazingira bora zaidi.

“Lengo la Serikali ni kuhakikisha wanafunzi wanapata mazingira mazuri ya kujifunzia ili waweze kufanya vizuri katika mitihani yao na kufikia ndoto zao,” amesema Mpogolo.

Aidha, ameeleza kuwa tangu mwaka 2007 shule hiyo ilikuwa ikikabiliwa na changamoto ya miundombinu, hali iliyosababisha wanafunzi kutumia vyumba  visivyokidhi mahitaji.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam,  ambaye pia ni Ofisa Elimu ya Sekondari wa halmashauri hiyo,Dk. Mussa Ally, amesema ujenzi wa madarasa hayo utaongeza ufanisi wa utoaji elimu na kusaidia wanafunzi kupata elimu bora.

Amesema Halmashauri itaendelea kutekeleza miradi ya maendeleo katika sekta ya elimu kuhakikisha changamoto za miundombinu zinapungua na wanafunzi wanapata fursa sawa za kujifunza.








Wananchi wa kata ya Magugu  iliyopo Wilaya ya Babati Mkoa wa Manyara wamemahukuru Mkuu wa Wilaya hiyo kwa kufanisha kutatua mgogoro uliodumu zaidi ya miaka (20).

Katika mgogoro huo, ilibainika kuwa baadhi ya wananchi walikuwa wamevamia eneo la mwekezaji katika maeneo ya vijiji vya Malangi na Kirusix, ambapo walikuwa wamejenga nyumba za kudumu pamoja na kuweka makaburi.

Katika juhudi za kutatua mgogoro huo, Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya alimshauri mwekezaji kukata sehemu ya eneo lake, hususan maeneo ambayo tayari wananchi wengi walikuwa wamejenga, ikiwemo Malangi na Kirusix.

Mwekezaji alikubali ombi hilo na kuamua kuachia sehemu ya eneo lake ili wananchi waweze kuishi kihalali.

Aidha, Mheshimiwa DC aliwaelekeza maafisa ardhi kwenda uwandani kwa ajili ya kupima eneo hilo lililotolewa kwa wananchi ambapo ilikubaini ukubwa wake pamoja na kuweka mipaka rasmi.

Vilevile, wananchi wote waliokuwa wamejenga katika eneo la mwekezaji walielekezwa kupewa viwanja katika eneo hilo jipya lililotengwa na kisha kuhamia huko rasmi.

Kwa upande mwingine, Mheshimiwa DC aliwataka wananchi kuishi kwa amani na kushirikiana katika kulinda mali za mwekezaji ili kudumisha uhusiano mzuri na maendeleo endelevu katika eneo hilo.












Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Katika hotuba yake ya makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Juma Homera, ametangaza mipango mikubwa inayolenga kuimarisha sekta ya sheria na haki nchini Tanzania. 

Mikakati hii ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha utawala bora, haki za binadamu, na upatikanaji wa haki kwa wote, huku lengo kuu likiwa ni kuimarisha huduma za kisheria, kuboresha mfumo wa haki, na kupunguza migogoro nchini.

Waziri huyo ameeleza kuwa moja ya vipaumbele vya wizara ni kuimarisha huduma za msaada wa kisheria, ili kuhakikisha kuwa wananchi wa rika zote wanapata haki zao, hususan katika maeneo ya vijijini ambako upatikanaji wa huduma za kisheria bado ni changamoto. 

Mikakati hii inalenga kutoa huduma za kisheria kwa urahisi na kuwafikia wananchi wengi, ili kuondoa vikwazo vya kimfumo ambavyo vimekuwa vikikwamisha upatikanaji wa haki. Katika hili, wizara itaweka mkazo kwenye kuimarisha huduma za kisheria katika ngazi ya jamii, ili wananchi wote waweze kupata msaada wa kisheria, bila kujali eneo wanalotoka au hali zao za kifedha.

Pamoja na huduma za msaada wa kisheria, wizara pia itaanza kuandaa Sera ya Haki Madai. Sera hii inalenga kuhakikisha kuwa wananchi wanapata haki zao kwa njia rahisi na yenye uwazi. Kwa kuanzisha mfumo huu, wizara inataka kuondoa urasimu na kuongeza uwajibikaji katika mchakato wa kudai haki, jambo ambalo litasaidia kupunguza malalamiko ya wananchi kuhusu ucheleweshaji wa haki. 

Sera ya Haki Madai itaimarisha mfumo wa kudai haki kwa wananchi, ikiwa ni pamoja na kuweka viwango vya juu vya uwazi na uwajibikaji katika mchakato wa utoaji haki, ambapo wananchi wataweza kufahamu hatua za kila mchakato wa kisheria na athari zinazotokana na hatua hizo.

Dkt. Homera alisisitiza pia umuhimu wa elimu katika kuimarisha utawala wa sheria. Wizara itatoa kipaumbele katika kueneza elimu ya Katiba na Haki Jinai, ambapo wananchi watafundishwa kuhusu haki zao, majukumu yao, na namna ya kujilinda dhidi ya ukiukwaji wa haki zao. Kupitia elimu hii, wizara inakusudia kuongeza uelewa wa umma kuhusu mifumo ya kisheria, ili wananchi wawe na uwezo wa kutumia haki zao kwa ufanisi. Elimu hii haitakuwa tu kwa raia wa kawaida bali pia kwa wadau wa kisheria, ili kuhamasisha uwazi na uwajibikaji katika utendaji wa majukumu ya kila mtu katika mfumo wa sheria.

Katika kuendeleza haki za binadamu, wizara itashirikiana na wadau mbalimbali ili kukuza haki za binadamu na biashara zinazohusiana na utawala wa sheria. Katika muktadha huu, wizara itahakikisha kuwa haki za binadamu zinaheshimiwa, na kwamba mifumo ya kisheria inafanya kazi kwa manufaa ya wananchi wote. 

Hii inajumuisha kutoa huduma za kisheria kwa makundi yaliyo hatarini, ikiwa ni pamoja na wanawake, watoto, na watu wenye ulemavu, ili kuondoa ubaguzi na kuhakikisha usawa kwa wote. Wizara pia itahakikisha kuwa haki za wanawake na watoto zinatambuliwa na kutekelezwa kwa ufanisi, ili kuzuia vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa kijinsia na kuhakikisha ulinzi wa haki za watoto.

Amesema Wizara itazidi kuimarisha mbinu mbadala za utatuzi wa migogoro (ADR) ili kupunguza migogoro inayotokea katika jamii. Kupitia utatuzi huu, wizara inatarajia kupunguza mzigo wa mashauri katika mahakama, na badala yake kuwezesha wananchi kupata suluhu za haraka na za amani kwa migogoro yao.

 Mbinu hizi pia zitachangia katika kujenga jamii yenye utulivu na usalama, ambapo migogoro inatatuliwa kwa njia zisizo za kimahakama. Hii itasaidia kuongeza ufanisi wa mfumo wa haki na kupunguza mzigo wa kesi katika mahakama, hivyo kutoa nafasi ya kumaliza mashauri kwa haraka na kwa usahihi.

Katika muktadha wa kupambana na uhalifu wa kimataifa, wizara itaendelea kutekeleza mikataba ya extradition kwa kushirikiana na nchi nyingine, ili kuhakikisha kuwa wahalifu wanaokimbia sheria hawapati kimbilio. 

Hatua hii ni muhimu katika kuhakikisha kuwa sheria za Tanzania zina nguvu hata nje ya mipaka ya nchi, na kwamba haki inapatikana kwa wahalifu wanaojificha katika mataifa mengine. Kwa kutekeleza mikataba hii ya kimataifa, Tanzania itaweza kushirikiana na nchi nyingine katika kupambana na uhalifu wa kimataifa, ikiwa ni pamoja na utakatishaji fedha na biashara haramu ya silaha.

Kwa lengo la kuhakikisha utekelezaji mzuri wa sheria na haki, wizara itaendelea kuimarisha uwezo wa taasisi zinazohusika na masuala ya sheria, pamoja na maafisa wa masuala ya rasilimali asilia. 

Hii itahakikisha kuwa wafanyakazi wa sekta ya sheria wanakuwa na ufanisi katika kutekeleza majukumu yao, na hivyo kusaidia kuimarisha huduma za kisheria kwa wananchi. Wizara pia itaboresha mifumo ya mafunzo na uwezo kwa maafisa wa serikali ili kuhakikisha kuwa wanatimiza majukumu yao kwa ufanisi na kwa kuzingatia haki za binadamu.

Kwa kuboresha usajili wa wosia na mirathi, wizara itahamasisha umma kujizatiti katika kuandika wosia na kuhakikisha kuwa mirathi inasimamiwa kwa uwazi. Hii ni hatua muhimu katika kupunguza migogoro inayotokana na usimamizi wa mali na urithi. 

Kupitia mikakati hii, wizara inatarajia kuboresha utawala wa sheria katika nyanja ya urithi, na kutoa suluhu ya kudumu kwa familia na vizazi vijavyo kuhusu usimamizi wa mali. Hii itasaidia kuondoa migogoro ya kifamilia inayotokana na utunzaji wa mali na kurithi, na kuleta usawa na haki katika usimamizi wa mali za familia.

Kwa ujumla, Wizara ya Katiba na Sheria inajizatiti katika kuleta mabadiliko makubwa katika sekta ya sheria na haki. Mikakati hii ya mwaka wa fedha 2026/2027 inalenga kuimarisha utawala wa sheria, kuboresha upatikanaji wa haki kwa wananchi, na kuhakikisha kuwa haki za binadamu zinatekelezwa ipasavyo. Kwa kutekeleza mikakati hii, Tanzania inajizatiti kuwa na jamii yenye utawala bora, haki, na usawa kwa wote.




Wadau mbalimbali wa elimu wakiwa katika mikutano na Wanafunzi wa baadhi ya Shule za wilayani Momba, ambapo maadhimisho ya Juma la Elimu Kitaifa yanafanyika.


MAADHIMISHO ya Juma la Elimu Kitaifa yanaendelea Mkoani Songwe ambapo TEN/MET na wadau wa Elimu nchini wametembelea shule ya wasichana ya Songwe, Wilayani Momba. Shule hiyo iliyoanza na wanafunzi 25 chini ya usimamizi wa mkoa, sasa imekua hadi kufikia idadi ya wanafunzi 161 na walimu 15 wenye dhamira thabiti ya kuinua elimu ya mtoto wa kike.

Akizungumza na wadau wa elimu, Mkuu wa Shule Bi. Janeth Mwamwile amesema kuwa kwa miaka minne mfululizo shule imepata ufaulu wa asilimia 100, na hivyo kung’ara katika ngazi ya wilaya, mkoa na hata taifa. Lakini pamoja na mafanikio hayo, amebainisha shule bado inakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo za miundombinu kama nyumba za walimu, maabara, bwalo la chakula, mabweni, jengo la utawala, jiko hivyo kutoa wito kwa wadau wa sekta ya elimu kuwashika mkono ili kuchochea mafanikio hayo.

Kwa upande wa Mtandao wa Elimu Tanzania @tenmet Bi. Martha Makala, Mratibu wa Mtandao), amesisitiza umuhimu wa kusaidia wasichana ili waweze kutimiza ndoto zao akitolea mfano wa Elimu yake aliyoipata kutoka shule ya wasichana kama chachu ya kufanikiwa maishani. Aidha, Bi. Makala ameahidi kuwa changamoto zilizobainishwa zimepokelewa na zitachakatwa ili kuona namna wadau wa TEN/MET wanavyoweza kushirikiana katika utatuzi wake.


WAKAZI zaidi ya 600 wa Dar es Salaam wamepewa siku 14 kulipa madeni ya pango la ardhi ili kuepuka kuchukuliwa hatua za kisheria.Kamishna Msaidizi wa Wizara ya Ardhi Mkoa huo, Shukrani Kyando, amesema hayo leo Aprili 24,2026  ambapo amesema kuwa wadaiwa hao tayari waliwahi kupewa notisi ya zaidi ya miezi mitatu pamoja na kukumbushwa mara kadhaa bila mafanikio.

“Kabla ya kufikia hatua ya kuwafikisha mahakamani, wizara imefuata taratibu zote za kibusara kwa kuwapa wadaiwa muda wa siku 14, siku 90, na sasa imeongeza tena siku 14 kuanzia Aprili 24, 2026.”

Kwa mujibu wa Kyando, yeyote atakayeshindwa kulipa ndani ya muda huo atafikishwa mahakamani kujibu mashitaka kwa mujibu wa sheria.
Amesisitiza kila mmiliki wa ardhi ana wajibu wa kulipa pango la ardhi kwa wakati, na kushindwa kufanya hivyo kunaweza kusababisha kupoteza haki ya umiliki pamoja na kukosa sifa za kupata mikopo.

“Mkoa wa Dar es Salaam ulikuwa na lengo la kukusanya shilingi bilioni 83, lakini hadi sasa zimekusanywa takribani shilingi bilioni 63, hali inayochelewesha kufikiwa kwa malengo ya asilimia 100.”
Kwa upande wake, Mratibu wa Kodi Mkoa huo, Alfred Thomas, amewataka wananchi kulipa kodi kwa wakati ili kulinda haki zao za msingi katika umiliki wa ardhi.


 

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amesema mradi wa ujenzi wa Maabara za Sayansi na Skuli ya Kilimo ya Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) ni muhimu kwa kuwa unaolenga kuweka misingi imara ya maendeleo ya Teknolojia, Ujuzi, na Uchumi katika jamii.

 Makamu wa Rais amesema hayo wakati akiweka Jiwe la Msingi la ujenzi wa Maabara za Sayansi na Skuli ya Kilimo ya Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) ikiwa ni shamrashamra za Miaka 62 ya Muungano.

 Amesema mradi huo utaleta manufaa makubwa kwa nchi, ikiwa ni pamoja na kutengeneza fursa za ajira, kuongeza uelewa katika sayansi na teknolojia, kushajihisha uchumi wa buluu na kuongeza tija katika kilimo.

 Aidha, Makamu wa Rais amesema elimu ni kipaumbele cha Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuwa ndiyo inayowezesha uendelezaji wa rasilimaliwatu ili kuchangia kikamilifu katika kujenga Taifa na kuleta maendeleo kwa ujumla. 

Ameongeza kwamba uwekaji wa Jiwe la Msingi unaangazia mafanikio ya Muungano wa Tanzania katika miaka 62 iliyopita, ambapo umewezesha kushirikiana zaidi, kuimarisha amani, na kustawisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika pande zote mbili za Muungano.

 Makamu wa Rais ametoa wito kwa Mshauri Elekezi na Mkandarasi wa mradi huo, kusimamia kikamilifu utekelezaji wa mradi na kuhakikisha unafikia malengo yaliyokusudiwa. Amesema ni matarajio kuona mradi unatekelezwa kwa kuzingatia viwango vya hali ya juu, weledi, thamani ya fedha na kukamilika kwa wakati.

Vilevile ametoa rai kwa uongozi wa SUZA kusimamia rasilimali hizo kwa uadilifu na uwazi ili kuhakikisha kuwa miundombinu inayojengwa inawezesha kufikiwa kwa malengo yaliyokusudiwa, ikiwemo kuchochea tafiti na bunifu zinazolenga kutatua changamoto halisi za jamii, hususan katika sekta za kilimo, teknolojia, utalii na mazingira. 

Kwa upande wake Kaimu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) Prof. Abdi Talib Abdalla amesema Jengo la Maabara ya Sayansi litakuwa kitovu muhimu katika ufundishaji wa sayansi tafiti za kisasa, bunifu na teknolojia ndani ya chuo na nchi kwa ujumla

 Amesema kupitia maabara hizo za kisasa wanafunzi na watafiti watapata mazingira bora ya kufanya majaribio tafiti shirikishi na bunifu zinazolenga kutatua changamoto mbalimbali za kijamii kiuchumi na kimazingira. 

Aidha uwekezaji huo utaongeza ubora wa elimu ya sayansi na kuzalisha wataalamu wenye ujuzi wa vitendo na uwezo wa kushindana katika soko la ajira la kitaifa na kimataifa.

 Pia amesema Maabara na Skuli ya Kilimo itaimarisha uwezo wa Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar katika kutoa huduma za ushauri elekezi, mafunzo maalum na tafiiti zinazolenga kutatua changamoto za jamii na kuchochea uchumi wa Taifa.

Mradi Maabara na Skuli ya Kilimo wa Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar umefadhiliwa na mradi wa Benki ya Dunia wa HEET (The Higher Education for Economic Transformation - HEET), ambapo unagharimu kiasi cha shilingi bilioni 32.155.





 

Na. Josephine Majura, WF, Dodoma

Serikali kupitia Mamlaka ya Mapato (TRA), itaendelea kutathmini na kufuatilia kwa karibu ukuaji wa mapato ya kodi, ongezeko la idadi ya walipakodi na shughuli za kiuchumi katika Wilaya ya Karatu, mkoani Arusha, ili pale vigezo vitakapokamilika hatua stahiki ziweze kuchukuliwa ikiwemo kuipandisha hadhi kuwa mkoa wa kikodi.

Hayo yameelezwa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum Mhe. Cecilia Paresso, aliyetaka kujua lini Serikali itaanzisha Mkoa wa Kikodi katika Wilaya ya Karatu.

Mhandisi Munde, alifafanua kuwa uanzishwaji wa mikoa ya kikodi hufanyika kwa kuzingatia vigezo vya kiutawala na kiuchumi ikiwemo kiasi cha mapato kinachokusanywa, idadi ya walipakodi, rasilimali zilizopo na mahitaji ya huduma katika eneo husika ili kuboresha utoaji wa huduma na kuongeza ufanisi wa ukusanyaji wa mapato ya kodi.

Aidha, alisema kuwa katika kuongeza ufanisi na kusogeza huduma kwa walipakodi, Serikali kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ilizipandisha hadhi baadhi ya wilaya za kikodi kuwa mikoa ya kikodi, ikiwemo Mkoa wa Kikodi wa Ilala, Kinondoni, Temeke, Kariakoo, Kahama, Tegeta na Pemba.

Mhandisi Munde, aliongeza kuwa Wilaya hizo zilizopewa hadhi ya mikoa ya kikodi zina wastani wa jumla ya walipakodi 906,399 (Ilala), 734,984 (Kinondoni), 563,568 (Temeke), 67,996 (Kariakoo), 82,054 (Kahama), 136,164 (Tegeta), na 28,076 (Pemba).

Kadhalika, katika mwaka wa fedha 2023/24 na 2024/25 wilaya hizo zilikuwa na wastani wa mapato ya kodi ya sh. bilioni 862.42 (Ilala), 574.36 (Kinondoni), 190.32 (Temeke), 136.03 (Kariakoo), 25.89 (Kahama), 101.1 (Tegeta), na 16.36 (Pemba).

“Kwa muundo wa kikodi wa sasa, Wilaya ya Karatu inatambulika kama wilaya ya kikodi chini ya mkoa wa kikodi wa Arusha ndani ya Idara ya Kodi za Ndani ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA)”, alisema Mhandisi Munde.

Wilaya ya Karatu ina jumla ya walipa kodi 4,672 ambao kwa kiasi kikubwa wanachangia ukusanyaji wa mapato ya kodi kutoka katika shughuli za utalii, madini na kilimo. Kadhalika, takwimu zinabainisha ukuaji wa asilimia 9.48 wa mapato ya kodi katika Wilaya hiyo, kwa kuzingatia makusanyo yenye jumla ya shilingi bilioni 10.07 kwa mwaka 2023/24 na sh. bilioni 11.12 kwa mwaka 2024/25.

Naibu Waziri wa Fedha Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum Mhe. Cecilia Paresso, aliyetaka kujua lini Serikali itaanzisha Mkoa wa Kikodi katika Wilaya ya Karatu, mkoani Arusha.

Serikali imewataka Wakaguzi Wakuu wa Migodi pamoja na Mameneja wa Migodi nchini kuwa mabalozi wa utekelezaji wa sheria, kanuni za madini na kuwa wazalendo katika biashara ya madini ili kuongeza mchango wa sekta hiyo kwenye uchumi wa taifa.

Wito huo umetolewa leo Aprili 24, 2026 wilayani Kahama, mkoani Shinyanga na Mtaalam kutoka Kurugenzi ya Ukaguzi na Biashara ya Madini  Tume ya Madini, Mhandisi Erasmina Massawe, kwenye mafunzo kwa Mameneja na Wakaguzi Wakuu wa Migodi ya uchimbaji mdogo yaliyowakutanisha washiriki kutoka mikoa ya kimadini ya Kahama, Mbogwe na Shinyanga.

Mafunzo hayo yamelenga kuimarisha uelewa wa kitaalam, usimamizi bora wa migodi, uzingatiaji wa sheria na kanuni za madini pamoja na kukuza uchimbaji salama na endelevu.

Amesema mbali na kujifunza mbinu za kuimarisha usalama migodini, viongozi hao wanapaswa kuwa sehemu ya mikakati ya Serikali ya kuhakikisha biashara ya madini inafanyika kwa uwazi na kwa kuzingatia Sheria ya Madini na kanuni zake, hatua itakayosaidia kudhibiti vitendo vya utoroshaji wa madini.

Ameeleza kuwa Serikali kupitia Tume ya Madini imeendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuimarisha usimamizi wa biashara ya madini, ikiwemo uboreshaji wa mfumo wa biashara ya madini, uanzishwaji wa masoko na vituo vya ununuzi wa madini, uwepo wa Maafisa Migodi Wakazi katika maeneo ya uchimbaji pamoja na ujenzi wa ukuta wa Mirerani uliosaidia kudhibiti utoroshaji wa madini ya Tanzanite.

Aidha, amesema Serikali imeimarisha ulinzi na ufuatiliaji wa madini kwa kuweka wakaguzi katika maeneo muhimu kama viwanja vya ndege, bandari, mipakani na katika maeneo yote ya uzalishaji madini, sambamba na kusimamia utoaji wa vibali vya usafirishaji wa madini na utekelezaji wa Sheria ya kodi ikiwemo ondoleo la Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kwenye baadhi ya shughuli za madini.

Akizungumzia uwezeshaji wa Watanzania kushiriki kikamilifu katika sekta hiyo, Mhandisi Massawe amesema maboresho ya Kanuni za Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini yameongeza kwa kiasi kikubwa ushiriki wa watanzania katika usambazaji wa bidhaa na  utoaji wa huduma mbalimbali migodini.

“Kwa sasa zipo fursa nyingi katika Sekta ya Madini ikiwemo huduma za chakula, ulinzi, vifaa kinga, huduma za kisheria, ujenzi na bima. Watanzania wanapaswa kuzitumia fursa hizi kujiongezea kipato na kukuza uchumi wa nchi,” amesisitiza.

Wakati huohuo amehimiza wadau wa madini nchini kutumia maabara bora ya Tume ya Madini iliyopo jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kupimiwa madini yao na sampluli za madini ili kufanya biashara ya madini ya uhakika.

Mafunzo hayo ni sehemu ya juhudi za Serikali kuimarisha usimamizi wa uchimbaji mdogo na kuhakikisha rasilimali za madini zinaleta manufaa mapana kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.






Top News