📍Ahimiza ulinza wa miundombinu na mapambano dhidi ya ukatili

NA MWANDISHI WETU, MBEYA

MKUU wa Wilaya ya Mbeya, Mhe. Solomon Itunda, amemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Beno Malisa, katika hafla ya uzinduzi wa Kituo cha Polisi cha Kata ya Igoma, kilichogharimu Shilingi milioni 150.

Hatua hiyo ni mkakati wa serikali kuimarisha ulinzi, usalama, na kusogeza huduma za kijamii karibu na wananchi.

Akizungumza katika uzinduzi huo uliokwenda sambamba na makabidhiano ya miundombinu hiyo, Mhe. Itunda amesema ujenzi wa kituo hicho ni matokeo ya juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kuboresha mazingira ya kazi ya vyombo vya ulinzi nchini.

Mhe. Itunda amebainisha kuwa uwekezaji huo mkubwa katika sekta ya usalama unalenga kudumisha amani na utulivu, mambo ambayo ni nguzo kuu katika kuchochea maendeleo ya kiuchumi ndani ya Mkoa wa Mbeya na taifa kwa ujumla.

Katika hatua nyingine, Mkuu huyo wa Wilaya ametoa onyo kali kwa watu wanaojihusisha na vitendo vya ukatili wa kijinsia.

Alisema serikali haitafanya muhali kwa yeyote atakayebainika kukiuka haki za wengine na amewataka wananchi kuwa mstari wa mbele kutoa taarifa za uhalifu kwa vyombo vya dola.

Aidha, Mhe. Itunda amewataka wakazi wa Igoma na maeneo jirani kukitunza kituo hicho kipya na kuona miundombinu hiyo kama mali yao, ili iweze kudumu na kutoa huduma kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

Amesisitiza kuwa ushirikiano kati ya polisi na jamii (Polisi Jamii) ndiyo silaha pekee ya kutokomeza uhalifu.

Uzinduzi huo umehudhuriwa na viongozi waandamizi wa Jeshi la Polisi, akiwemo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya (RPC), Benjamin Kuzaga, pamoja na Mkuu wa Polisi Wilaya ya Kipolisi Mbalizi (OCD), ambao kwa pamoja wameahidi kuongeza ufanisi wa kazi kutokana na kupatikana kwa kituo hicho kipya.





Wanafunzi wajasiriamali ishirini kutoka vyuo vikuu mbalimbali nchini wamepatiwa zawadi za fedha taslimu zaidi ya Shilingi milioni 70 kufuatia shindano la uwasilishaji wa mawazo ya biashara lililofanyika chini ya mpango wa Youth Ignite Student Founders Fellowship – Awamu ya Pili, unaotekelezwa kupitia Programu ya FUNGUO iliyo chini ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Maendeleo (UNDP) nchini Tanzania, kwa ufadhili wa pamoja wa Serikali ya Uingereza - kupitia Ofisi ya Mambo ya Nje, Jumuiya ya Madola na Maendeleo ya Uingereza (FCDO), Umoja wa Ulaya (EU) na serikali ya Finland.

Hafla hiyo ya uwasilishaji wa mawazo ya biashara iliwakutanisha pamoja wanafunzi 30 kutoka taasisi za elimu ya juu kutoka vyuo tofauti Tanzania, waliowasilisha mawazo bunifu ya biashara yenye mchango chanya kwa jamii mbele ya jopo la majaji. Tukio hili limekuwa hatua muhimu katika kuimarisha ujasiriamali na ubunifu miongoni mwa vijana nchini. Mbali na ushindi wa zawadi za fedha taslimu, wanafunzi wajasiriamali pia walipokea msaada wa kitaalamu, ikiwemo mafunzo ya maendeleo ya biashara, ushauri elekezi (mentorship), na maandalizi ya kuwafanya wawe tayari kuvutia wawekezaji wapya.

Mgeni Rasmi, Dkt. Harun Makandi, Mkurugenzi Msaidizi wa Sayansi na Teknolojia kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, alisisitiza jinsi mpango huo unavyoendana na ajenda ya Serikali ya kukuza ubunifu, utafiti wenye tija kibiashara, na ujasiriamali miongoni mwa vijana.

“Mpango huu unaunga mkono moja kwa moja jitihada za serikali za kulea kizazi kipya cha wabunifu na wazalishaji wa ajira mpya kinachotoka katika taasisi zetu za elimu ya juu. Unaakisi mwelekeo wa Tanzania wa kuunganisha sayansi, teknolojia na ujasiriamali katika maendeleo ya taifa,” alisema Dkt. Makandi.

Akitoa hotuba kuu, John Rutere, Naibu Mwakilishi Mkazi wa UNDP Tanzania, alieleza jinsi ushirika huo unavyochangia malengo ya muda mrefu ya maendeleo ya Tanzania.

“Jukumu la UNDP nchini Tanzania limejikita katika kuunga mkono Dira ya Maendeleo ya Tanzania 2050 (DIRA 2050), ambayo imeweka lengo la kuifanya Tanzania kuwa nchi ya kipato cha kati cha juu kwa kufikia kiwango cha uchumi wenye thamani ya Dola za Kimarekani Trilioni moja ifikapo mwaka 2050. Kufikia dira hii kunahitajika uwekezaji wa makusudi kwa vijana na biashara zao. Programu kama Youth Ignite Student Founders Fellowship ni mifano halisi ya miradi iayoongeza chachu inayowawezesha vijana kwa ujuzi, mitandao ya wawekezaji na mitaji wanayohitaji kujenga biashara zenye uwezo wa kukua na kuchangia kwa kiasi kikubwa katika ukuaji wa uchumi wa taifa.”

Washirika wa maendeleo walichangia kwa kiasi kikubwa kufanikisha kundi hili la washiriki. Bw. Euan Davidson, Kiongozi wa Timu ya Miradi Endelevu katika Ofisi ya Mambo ya Nje, Jumuiya ya Madola na Maendeleo ya Uingereza (FCDO), alizungumza kwa niaba ya juhudi za maendeleo za Uingereza, akisisitiza umuhimu wa kuwekeza katika biashara zinazoongozwa na vijana kama kichocheo cha ukuaji wa uchumi jumuishi.

Westerwelle Foundation Tanzania na StartHub Africa zilichangia programu kwa kuwapatia washiriki ujuzi wa vitendo wa ujasiriamali, ikiwemo mafunzo ya kuandaa na kuwasilisha wazo la biashara (pitch development) na mawasilisho ya biashara, ili kuhakikisha wanakuwa tayari kuvutia uwekezaji kabla ya mashindano.

Naye Bi. Sanna-Liisa Taivalmaa, Mkuu wa Ushirikiano katika Ubalozi wa Finland, alihutubia hafla hiyo na kuthibitisha dhamira ya Finland kuendelea kuunga mkono mifumo ya ubunifu na ujasiriamali wa vijana kama sehemu ya vipaumbele vya ushirikiano wa maendeleo.

Miongoni mwa washindi waliofanya vizuri zaidi kila mmoja alipokea kiasi cha Shilingi milioni 6 kwa ajili ya kukuza biashara zao.

Herriet Nairumbe, Mwanzilishi wa Niches Food Products yenye makao Arusha, anajihusisha na uongezaji thamani wa mazao ya pilipili na matunda. Akizungumza baada ya kutangazwa mshindi, alieleza jinsi fedha hizo zitakavyosaidia kukuza kampuni yake.

“Fedha hizi zitatumika kununua mashine itakayorahisisha uzalishaji na kuongeza tija. Pia tunapanga kuwekeza katika masoko ya mikoa mingine ili watu wengi zaidi wafahamu bidhaa zetu,” alisema.

Herriet pia alizungumzia changamoto za ushindani wanazokutana nazo wajasiriamali wachanga sokoni.

“Changamoto kubwa kwa biashara mpya ni kulinganishwa na bidhaa za kampuni zilizoimarika na zinazojulikana. Kupitia programu ya Youth Ignite Student Founders Fellowship, tumeimarisha msingi wa biashara yetu. Tumejifunza utunzaji wa kumbukumbu za mahesabu, upangaji wa bei za bidhaa, ujenzi wa timu, na huduma kwa wateja — mambo ambayo yanatusaidia kupata na kuwafanya wateja wadumu zaidi.”

Aliongeza kuwa programu hiyo imekuwa muhimu katika kuhakikisha biashara yao inakuwa endelevu na inatoa ajira kwa vijana wengine.

“Ninaishukuru programu hii kwa sababu imeimarisha uimara wa biashara yetu na kutuwezesha kutengeneza ajira zaidi kwa vijana.”

Mshindi mwingine alikuwa ni Irene George Ngatibigwa, Mwanzilishi Mwenza wa Eco Mushroom, kampuni inayojihusisha na uzalishaji wa uyoga mbichi, uliokaushwa, unga wa uyoga na vitafunwa vinavyotokana na uyoga. Alieleza jinsi changamoto za miundombinu zilivyomzuia kupanua biashara mwanzoni.

“Nilipoanza, changamoto yangu kubwa ilikuwa ukosefu wa miundombinu ya kupanua uzalishaji na kufikia soko kubwa zaidi. Nilikuwa napata oda lakini sikuweza kuingia mikataba kwa sababu sikuwa na uwezo wa kukidhi mahitaji ya usambazaji.”

Irene alisema fedha alizopata zitasaidia kuongeza uwezo wa uzalishaji na kupanua ajira.

“Hizi Shilingi milioni 6 zitanisaidia kununua vifaa, kuboresha miundombinu ya uzalishaji, na kuajiri vijana zaidi katika uzalishaji na masoko.”

Akizungumzia baada ya kushiriki programu hiyo, alibainisha mabadiliko makubwa katika mtazamo wake wa kibiashara.

“Kabla ya kujiunga na Youth Ignite Student Founders Fellowship, nilikuwa nafanya biashara kwa mapenzi binafsi tu bila ujuzi rasmi kama vile masoko au namna ya kuwashawishi wawekezaji wapya. Kupitia mafunzo, nimejifunza masoko, uwasilishaji kwa wawekezaji, na kujenga mitandao na wawekezaji. Ujuzi huu utakuwa muhimu sana tunapokuza na kupanua biashara yetu.”

Kupitia ushauri elekezi, mafunzo na msaada wa kifedha, Youth Ignite Student Founders Fellowship inaendelea kujenga kizazi cha biashara za wanafunzi zenye uwezo mkubwa wa kukua na kuchangia katika mabadiliko ya kiuchumi ya Tanzania.

Washindi wanawakilisha sekta mbalimbali zikiwemo teknolojia, kilimo-biashara, suluhisho za mabadiliko ya tabianchi, uzalishaji viwandani, na ubunifu wa kijamii — jambo linaloonesha upana wa mawazo bunifu yanayotoka katika taasisi za elimu ya juu nchini.

Programu ya FUNGUO ya UNDP inachochea ubunifu nchini Tanzania kwa kuendesha ukuaji wa uchumi kupitia kulea wajasiriamali, kuwezesha upatikanaji wa ufadhili, na kukuza ushirikiano wenye matokeo chanya. Kwa pamoja, tunaunda suluhisho endelevu kwa changamoto za leo. Ikipewa ufadhili wa pamoja na Umoja wa Ulaya, Serikali ya Uingereza, serikali ya Finland, na UNDP, FUNGUO inasaidia kuondoa vikwazo ndani ya mfumo wa ubunifu wa Tanzania. Kuanzia ufadhili mpaka ushauri elekezi, tunawezesha biashara changa na ndogo kwa zana na rasilimali wanazohitaji ili kukua, kustawi, na kuleta athari chanya ya kudumu.

Dkt. Harun Makandi, Mkurugenzi Msaidizi wa Sayansi na Teknolojia kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia (wa tatu kushoto), akimkabidhi mfano wa hundi mmoja wa washindi walioshika nafasi ya kwanza wa programu ya Youth Ignite Student Founders Fellowship – Msimu wa Pili, Bi. Herriet Nairumbe, Mwanzilishi wa Niches Food Products yenye makao yake Arusha. Wanaoshuhudia tukio hilo upande wake wa kulia ni John Rutere, Naibu Mwakilishi Mkazi wa UNDP Tanzania, na Bi. Shakila Mshana, Mwanzilishi Mwenza na Mkurugenzi Mtendaji wa StartHub Africa; huku upande wa kushoto kabisa wakiwa Bi. Sanna-Liisa Taivalmaa, Mkuu wa Ushirikiano katika Ubalozi wa Finland, na Joseph Manirakiza, Meneja wa Programu ya FUNGUO, UNDP Tanzania.


John Rutere, Naibu Mwakilishi Mkazi wa UNDP Tanzania, akitoa pongezi wakati wa hafla ya kukabidhi vyeti kwa mmoja wa washindi wakuu wa programu ya Youth Ignite Student Founders Fellowship – Msimu wa Pili iliyofanyika Dar es Salaam mwishoni mwa wiki. Wanaoshuhudia tukio hilo upande wake wa kushoto ni Dkt. Harun Makandi, Mkurugenzi Msaidizi wa Sayansi na Teknolojia kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, pamoja na Joseph Manirakiza, Meneja wa Programu ya FUNGUO, UNDP Tanzania.





Dkt. Harun Makandi, Mkurugenzi Msaidizi wa Sayansi na Teknolojia kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia (wa tatu kushoto), akimkabidhi mfano wa hundi mmoja wa washindi walioshika nafasi ya pili wa programu ya Youth Ignite Student Founders Fellowship – Msimu wa Pili iliyofanyika Dar es Salaam mwishoni mwa wiki. Wanaoshuhudia tukio hilo upande wake wa kulia ni John Rutere, Naibu Mwakilishi Mkazi wa UNDP Tanzania, na upande wa kushoto kabisa ni Bi. Sanna-Liisa Taivalmaa, Mkuu wa Ushirikiano katika Ubalozi wa Finland, pamoja na Joseph Manirakiza, Meneja wa Programu ya FUNGUO, UNDP Tanzania.























Standard Chartered Tanzania imeongeza dhamira yake ya kuunga mkono ubunifu wa ndani na uwezeshaji wa kiuchumi kwa kutangaza mchango wa USD 11,500 kwa Challenges Worldwide Tanzania. Challenges Worldwide ni mshirika mkuu wa utekelezaji wa programu ya RISE/E ya Taasisi ya Standard Chartered.

Fedha hizi zimeelekezwa mahsusi katika kuimarisha ujuzi wa wajasiriamali wa ndani, huku mkazo maalum ukiwekwa kwa watu wenye ulemavu.

Mchango huo kwa mpango unaoitwa Wazo Bora Pitch utawezesha kambi ya mafunzo ya wiki moja, iliyobuniwa na kutekelezwa na Challenges Worldwide. Baada ya kukamilika kwa mafunzo haya, washiriki watapata fursa ya kuwasilisha mipango yao iliyoboreshwa ya biashara mbele ya jopo la majaji. Majaji watachagua washindi wa kwanza, wa pili na wa tatu ambao watapatiwa mtaji wa kuanzisha na kupanua miradi yao.

Standard Chartered Tanzania inaendelea kujikita katika kuinua wajasiriamali. Jitihada hizi ni sehemu ya mpango mpana wa miaka mitatu wenye thamani ya TZS bilioni 2.2 — mpango wa RISE/E — uliozinduliwa mwaka 2024 kupitia Taasisi ya Standard Chartered. Lengo kuu la mpango huu ni kusaidia moja kwa moja biashara ndogo 340 na kuzalisha nafasi 478 za ajira mpya.

Mwakilishi wa Benki alisema: “Tunaendelea kufanya kazi na wadau muhimu kama Challenges Worldwide ili kuleta mabadiliko yenye maana katika jamii zetu. Mchango huu wa hivi karibuni unahakikisha tunakuza uwezeshaji endelevu wa kiuchumi kwa kuwaongezea wajasiriamali wa ndani mtaji na ujuzi wanaohitaji kufanikiwa.”


Mgombea wa nafasi ya Ubunge Jimbo la Peramiho kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. Lazaro Komba Bunungu, amechukua rasmi fomu ya kuomba ridhaa ya kugombea ubunge katika jimbo hilo lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea.

Akizungumza mara baada ya kuchukua fomu hiyo, Dkt. Bunungu amesema amejiandaa kikamilifu kuwatumikia wananchi wa Jimbo la Peramiho endapo atapewa ridhaa hiyo na wananchi.

 Ameeleza kuwa dhamira yake ni kushirikiana na wananchi katika kuwaletea maendeleo ya kijamii na kiuchumi kupitia sera na mwelekeo wa Chama Cha Mapinduzi.

Aidha, amewashukuru wananchi wa Peramiho kwa sapoti na ushirikiano wao, huku akiwataka kuendelea kudumisha mshikamano na umoja wakati wa mchakato wa uchaguzi.

 Vilevile, amekishukuru Chama Cha Mapinduzi Taifa kwa imani waliyoonesha kwake kwa kumpa ridhaa kupeperusha bendera ya CCM katika uchaguzi mdogo Peramiho

Kwa upande wake, Katibu wa CCM Songea Vijijini, Juma Nambaila, amewashukuru viongozi wa CCM kutoka kata zote 16 za jimbo hilo kwa mshikamano wao, akisema hali hiyo ni ishara ya ushindi wa chama hicho katika uchaguzi unaotarajiwa kufanyika tarehe 26 Februari.

Naye Mwenyekiti wa CCM Songea Vijijini, Thomas Masolwa, amempongeza Dkt. Bunungu kwa kuchukua fomu hiyo, akisema CCM imemuamini kuwa msimamizi wa masuala ya maji, umeme na barabara, pamoja na kuwa sauti ya wananchi wa Peramiho.













 

Waziri wa Fedha wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb.), ameielekeza Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) kuelekeza mipango na mikakati yake zaidi katika kuendeleza kilimo cha mazao ya chakula na biashara yenye thamani kubwa katika soko la kimataifa, ili kuongeza kipato cha wakulima, wafugaji na wavuvi pamoja na kukuza mchango wa sekta hizo katika uchumi wa taifa.

Aidha, Waziri huyo amesisitiza umuhimu wa kuwekeza katika mazao ya misitu ikiwemo ufugaji wa nyuki, akieleza kuwa sekta hiyo ina fursa kubwa ya kiuchumi na mchango katika uhifadhi wa mazingira na maendeleo endelevu.

Ushauri huo umetolewa leo, Februari 1, 2026, Jijini Dodoma, wakati Waziri wa Fedha alipokutana na kufanya mazungumzo na ujumbe wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania ulioongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa TADB, Bw. Frank Nyabundege, ambapo pia alipokea taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya Benki hiyo.

Katika mazungumzo hayo, Balozi Omar ameahidi kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na TADB katika utekelezaji wa mikakati yake ya muda wa kati, kwa lengo la kuongeza tija na mchango wa sekta za kilimo, mifugo na uvuvi katika maendeleo ya kiuchumi ya nchi.

Pamoja na hayo, Waziri wa Fedha ameipongeza TADB kwa ufanisi wake wa kiutendaji na mchango wake mkubwa katika kuchochea maendeleo jumuishi na endelevu, hususan katika sekta za kilimo, mifugo, uvuvi pamoja na viwanda vya kuchakata mazao ya kilimo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TADB, Bw. Frank Nyabundege, amesema Benki hiyo imeendelea kukua kwa kasi kifedha, ambapo mizania yake imeongezeka kutoka shilingi bilioni 362.8 mwaka 2021 hadi kufikia shilingi trilioni 1.3 mwaka 2025.

Bw. Nyabundege amesema kuwa tangu kuanzishwa kwa Benki hiyo mwaka 2015, TADB imefanikiwa kutoa mikopo yenye thamani ya zaidi ya shilingi trilioni 1.3 kwa wakulima, wafugaji na wavuvi, hatua iliyochangia kuimarisha uzalishaji na kuongeza thamani katika mnyororo wa sekta ya kilimo nchini.

Ametoa shukrani kwa Serikali kupitia Wizara ya Fedha kwa kuiwezesha Benki hiyo kwa mtaji, akieleza kuwa hatua hiyo inaonesha dhamira na utashi wa kisiasa wa Serikali ya Awamu ya Sita katika kuikuza na kuiendeleza sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi.

Hata hivyo, Mkurugenzi Mtendaji huyo ameiomba Serikali kuendelea kuiwezesha TADB kimtaji kupitia bajeti kuu ya Serikali pamoja na kuidhamini Benki hiyo ili iweze kufikia masoko ya kimataifa ya mitaji, kwa lengo la kuongeza uwezo wa kutoa mikopo kwa wakulima na wadau wengine wa sekta ya kilimo.
  











Na Mwandishi wetu- Dodom.

Waziri wa Uchukuzi Prof Makame Mbarawa amesema Wizara imekamilisha taratibu za kuanza upanuzi mkubwa wa Bandari ya Dar es Salaam wenye lengo la kujenga magati 10 pamoja na matenki 15 ya mafuta.

 Ujenzi wa magati mawili (2) ya awali yenye urefu wa mita 500 utaanza mwezi Juni, 2026 na huku ujenzi wa matenki ukiendelea kutekelezwa kwa mafanikio makubwa. 

Prof Mbarawa ameyabainisha hayo leo jijini Dodoma kwenye  Mkutano na Waandishi wa habari akieleza utekelezaji wa siku 100 za Serikali ya awamu ya sita kipindi Cha pili.

"Uboreshaji huu utaongeza uwezo wa Bandari ya Dar es Salaam kuhudumia shehena hadi tani milioni 50 kwa mwaka ndani ya kipindi kifupi, kutoka takribani tani milioni 32 za sasa"

Amesema  kuanza kwa maandalizi ya ujenzi wa Bandari kubwa na ya kisasa ya Bagamoyo, Awamu ya Kwanza ya mradi huo itahusisha ujenzi wa gati lenye urefu wa kilometa 1.32 kwa ajili ya kuhudumia meli kubwa za kisasa (Mega Max). 

Bandari hiyo ni ya kimkakati katika kupunguza msongamano wa Bandari ya Dar es Salaam na kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha usafirishaji wa baharini katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Aidh Prof Mbarawa amesema katika hatua nyingine za kuendeleza huduma za bandari nchini, Serikali imeanza utekelezaji wa Mradi wa Kurasini Logistics Terminal, unaolenga kupunguza msongamano wa shehena katika Bandari ya Dar es Salaam na kuongeza miundombinu muhimu ya kuhudumia shehena inayoharibika haraka (perishables). 

Hat hivyo Prof Mbarawa amesema Mradi huo unahusisha ujenzi wa kituo cha kisasa cha kuhifadhi makasha kwa muda katika eneo la mita za mraba 210,000, chenye uwezo wa kuhifadhi hadi makasha 700,000.

Aidha  Prof Mbarawa ameelez kuwa kwa sasa, Awamu ya Kwanza ya ujenzi katika eneo la mita za mraba 81,000 inaendelea; 

Wizara imekamilisha maboresho ya Bandari za Kemondo na Bukoba katika Ziwa Victoria na bandari hizi zinatarajiwa kuwa kitovu muhimu cha usafirishaji kati ya Bukoba, Mwanza na bandari za Uganda.

"Hatua hii itaongeza biashara ya kikanda na kupunguza gharama za usafiri kwa njia ya maji;

Katika hatua nyingine, Serikali kupitia TPA inaendelea na ujenzi wa  bandari ya Kisiwa Mgao  Mtwara mradi ambao ni maalum kwa ajili ya kuhudumia shehena ya mzigo mchafu (Dirty Cargo) kama vile Makaa ya Mawe na Saruji. Kwa sasa, Mkandarasi anaendelea na utekelezaji wa mradi huu ambao hadi sasa umefikia asilimia 18 ya utekelezaji"

Hata hivyo amesema mukamilika kwa mradi huo kutaongeza ufanisi katika utendaji wa Bandari ya Mtwara na vile vile uimarishaji na utunzaji wa mizigo katika Ziwa Nyasa, Serikali kupitia TPA inaendelea kutekekeza mradi wa Ujenzi wa Bandari ya Mbamba Bay unaohusisha ujenzi wa gati ya kuhudumia shehena ya magari (RO-RO) na meli, jengo la Utawala, Uzio, Barabara, Jengo la Kuhifadhia Mizigo pamoja na Jengo la Abiria. Mradi huu kwa sasa umefikia asilimia 46 ya utekelezaji wake.




 

NA EMMANUEL MBATILO, MICHUZI TV

KLABU ya Simba imelazimishwa sare 2-2 na Esperance de Tunis katika mchezo wa hatua ya makundi ligi ya mabingwa Afrika.

Katika mchezo huo Simba Sc ilifanikiwa kuongoza kwa mabao 2-0 kipindi cha kwanza kupitia kwa Shomari Kapombe na Yusuf Kagoma na kwenda mapumziko wa wakiwa mbele.

Kipindi cha pili Esperance de Tunis waliingia wakilisaka lango la Simba sc nakufanikiwa kupata bao la kwanza baada ya Lassane Kante kutoa basi ambayo ilimpata mpinzani na kwenda kufunga bao ambalo liliwapa matumaini na kufanikiwa kupata bao la pili.

Kwenye mchezo huo pia Esperance de Tunis walipata penati dakika ya za mwisho wa mchezo lakini penati hiyo hawakuweza kupata bao.



Top News