Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndg. Asha-Rose Migiro, leo tarehe 21 Aprili 2026 amekutana na kufanya mazungumzo na ujumbe wa Mtandao wa Viongozi Wanawake wa Afrika (African Women Leaders Network - AWLN), ulioongozwa na Marais wastaafu wa Jamhuri ya Liberia, Mhe. Ellen Johnson Sirleaf, na Jamhuri ya Shirikisho la Kidemokrasia ya Ethiopia, Mhe. Sahle-Work Zewde, jijini Dar es Salaam.

Mazungumzo hayo yalijikita katika hali ya kisiasa nchini pamoja na matukio ya wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025, yakihusisha pia umuhimu wa kudumisha amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa.

Ujumbe huo upo nchini Tanzania kwa ziara ya kikazi yenye lengo la kufanya mashauriano na viongozi mbalimbali wa kitaifa kuhusu maendeleo ya kisiasa na juhudi zinazoendelea za kuimarisha demokrasia na utawala bora, ikiwa ni sehemu ya mchango wa wanawake viongozi wa Afrika katika kulinda amani na utulivu barani.






Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akitoa heshima za mwisho kwa mwili wa Askofu wa Jimbo Katoliki Kondoa, marehemu Askofu Bernadin Francis Mfumbusa, mara baada ya Ibada ya kumuaga na kumuombea iliyofanyika Katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Paulo wa Msalaba , Jimbo Kuu Katoliki Dodoma, leo tarehe 21 Aprili 2026.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akiwasili Katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Paulo wa Msalaba , Jimbo Kuu Katoliki Dodoma, kushiriki Ibada ya kumuaga na kumuombea Askofu wa Jimbo Katoliki Kondoa, marehemu Askofu Bernadin Francis Mfumbusa, leo tarehe 21 Aprili 2026.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akishiriki Ibada ya kumuaga na kumuombea Askofu wa Jimbo Katoliki Kondoa, marehemu Askofu Bernadin Francis Mfumbusa, iliyofanyika Katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Paulo wa Msalaba , Jimbo Kuu Katoliki Dodoma, leo tarehe 21 Aprili 2026.






Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akitoa salamu za rambirambi mara baada ya Ibada ya kumuaga na kumuombea Askofu wa Jimbo Katoliki Kondoa, marehemu Askofu Bernadin Francis Mfumbusa, iliyofanyika Katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Paulo wa Msalaba , Jimbo Kuu Katoliki Dodoma, leo tarehe 21 Aprili 2026.

MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amesema Taifa litaukumbuka mchango mkubwa aliyoutoa marehemu Askofu Bernadin Mfumbusa, enzi za uhai wake ikiwemo kuwa kiungo muhimu wa kuunganisha Kanisa Katoliki na Madhehebu mbalimbali pamoja na Dini zingine.

Makamu wa Rais amesema hayo mara baada ya kushiriki Ibada ya kumuaga na kumuombea Askofu wa Jimbo Katoliki Kondoa, marehemu Askofu Bernadin Francis Mfumbusa, iliyofanyika Katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Paulo wa Msalaba, Jimbo Kuu Katoliki Dodoma.

Amesema Marehemu Askofu Mfumbusa alijitolea katika kuunganisha dini na madhehebu ili zifanye kazi kwa kuheshimiana, kushirikiana na kupendana. Ameongeza kwamba Taifa litakumbuka mchango wake katika kuhamasisha elimu pamoja na kufanya kazi kubwa ya kuhamasisha na kusimamia ujenzi na uendelezaji wa huduma za Afya katika Wilaya ya Kondoa na Taifa kwa ujumla.

Makamu wa Rais amesema Marehemu Askofu Mfumbusa ametoa mchango katika sekta ya Mawasiliano na Habari akiwa mbobezi na mwalimu katika fani hiyo. Amesema Marehemu Mfumbusa atakumbukwa kwa kutimiza wajibu wake kwa binadamu kwa kutambua Maisha tunayoishi leo, na kutimiza wajibu wake kwa Mungu kwa kutuongoza katika njia ya uzima wa milele.

Aidha Makamu wa Rais amewasilisha salamu za pole za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, alizotoa kwa Kanisa, Waumini na Familia na kuiombea familia nguvu na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu.

Makamu wa Rais amewashukuru Viongozi wa Kanisa Katoliki kwa malezi ya marehemu Askofu Mfumbusa ambayo yalimfanya kuwa mtume wa Taifa zima.

Ibada hiyo, imeongozwa na Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki Dodoma Mhashamu Wilbroad Kibozi na kuhudhuriwa na Maaskofu mbalimbali, Mapadre, Watawa, Viongozi mbalimbali wa Serikali na Wananchi.

Imetolewa na
Ofisi ya Makamu wa Rais
21 Aprili 2026
Dodoma.



Na Mwamvua Mwinyi, Kibaha Aprili 21, 2026
KIONGOZI wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2026, Wazo Mwang’onda, ameweka jiwe la msingi katika kiwanda cha Doweicare Technology Ltd kilichopo Kata ya Misugusugu, Manispaa ya Kibaha, huku akiipongeza Serikali kwa kuweka mazingira rafiki kwa wawekezaji.

Kiwanda hicho kinajishughulisha na utengenezaji na usambazaji wa bidhaa za softcare kwa matumizi ya usafi, ikiwemo nepi za watoto na taulo za kike, kikiwa kimewekeza dola za Marekani milioni 16, sawa na takribani shilingi bilioni 40.

Akikagua na kuweka jiwe la msingi katika kiwanda hicho Aprili 21, 2026, Mwang’onda aligawa taulo za kike 6,000 kwa wanafunzi 1,000, zitakazowatosheleza kwa muda wa miezi sita.

Aidha, aliipongeza Manispaa ya Kibaha pamoja na Mkuu wa Wilaya hiyo kwa kuendelea kumpa ushirikiano Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kusimamia na kuimarisha sekta za uwekezaji na viwanda.

Awali, akipokea Mwenge wa Uhuru katika viwanja vya Shule ya Msingi Visiga, Kata ya Visiga, Manispaa ya Kibaha, Mkurugenzi wa Manispaa hiyo, Dkt. Rogers Shemwelekwa, alisema miradi nane yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 41.1 imezinduliwa, kukaguliwa na kuwekwa mawe ya msingi.

Miradi hiyo ni ujenzi wa barabara ya Kongowe–Forest, ujenzi wa vyumba vya madarasa katika Shule ya Sekondari Picha ya Ndege, na huduma za afya katika Zahanati ya Kilimahewa yenye thamani ya shilingi milioni 284.6.

Miradi mingine ni kisima kirefu cha maji safi katika Shule ya Msingi Tangini, mradi wa Kibaha Shopping Mall pamoja na mradi wa CJ-Chalya Plumbing Services unaohusisha shughuli za kikundi katika utengenezaji na uuzaji wa mabomba ya maji.

Mwenge wa Uhuru upo katika siku ya nne tangu kupokelewa mkoani Pwani Aprili 18, 2026, na unatarajiwa kupokelewa wilayani Mafia Aprili 22, 2026.




Na Mwandishi Wetu

Jumba la sanaa la Rangi Gallery la jijini Dar es Salaam limeandika historia baada ya kuwa taasisi ya kwanza kutoka Tanzania kushiriki katika maonesho ya kimataifa ya sanaa ya Art OnO 2026 yaliyofanyika jijini Seoul, Korea Kusini.

Maonesho hayo yaliyofanyika kuanzia Aprili 2 hadi 5 mwaka huu katika kituo cha maonesho cha SETEC, yameelezwa kuwa miongoni mwa majukwaa makubwa na yenye hadhi ya juu barani Asia yanayowakutanisha wadau wa sanaa kutoka mataifa mbalimbali duniani.

Kupitia ushiriki huo, Rangi Gallery ilisimama sambamba na majumba makubwa ya sanaa kutoka nchi 12 zikiwemo Japan, Ujerumani, Uswisi na mataifa mengine, hatua iliyotajwa kuiweka Tanzania katika ramani ya sanaa ya kisasa duniani.

Katika maonesho hayo, Rangi Gallery iliwasilisha kazi za wasanii wanne wanawake kutoka Tanzania ambao ni Theresia Venance, Tulsi Patel, Valerie Asiimwe Amani na Turakella Editha Gyindo.

Kazi za wasanii hao zilionesha upekee wa sanaa ya kisasa ya Kitanzania, zikigusa masuala ya utambulisho, mila, mabadiliko ya kijamii, uzoefu wa mwanamke pamoja na uhusiano wa binadamu na mazingira.

Mwanzilishi na Mkurugenzi Mtendaji wa Rangi Gallery, Lorna Mashiba Albou, alisema ushiriki huo ni ushahidi kuwa sanaa ya Tanzania ina uwezo mkubwa wa kushindana kimataifa.

“Wasanii wetu wameiwakilisha vyema Tanzania katika jukwaa hili la kimataifa. Hii inaonesha vipaji vya Kitanzania vinaweza kufika mbali vikipewa nafasi sahihi,” alisema Lorna.
Aliongeza kuwa licha ya wasanii wote waliowasilishwa kuwa wanawake, jambo hilo halikupangwa mahsusi bali lilitokana na ubora wa kazi zao.

Ushiriki wa Rangi Gallery pia umepewa uzito wa kidiplomasia baada ya Balozi wa Tanzania nchini Korea Kusini, Togolani Edriss Mavura, kuhudhuria maonesho hayo na kushuhudia kazi zilizooneshwa.

Wadau wa sanaa wameeleza kuwa hatua hiyo ni mwanzo wa safari kubwa kwa Tanzania katika soko la kimataifa la sanaa, huku baadhi ya wasanii walioshiriki wakitarajiwa kuiwakilisha nchi katika maonesho makubwa ya Venice Biennale 2026 nchini Italia.

Rangi Gallery ilianzishwa jijini Dar es Salaam na Lorna Mashiba Albou, ambaye awali alikuwa mwanasheria kabla ya kuhamia katika sekta ya uchumi wa ubunifu.

Mbali na kuonesha kazi za wasanii wa ndani, jumba hilo linaendesha programu ya Rangi Nyumbani Residency, inayolenga kuwaunganisha wasanii wa Tanzania na mitandao ya kimataifa.

Wachambuzi wanasema Tanzania imekuwa na vipaji vingi vya sanaa kwa miaka mingi, lakini changamoto kubwa imekuwa ukosefu wa majukwaa ya kuvitangaza. Kupitia juhudi za taasisi kama Rangi Gallery, sasa mlango wa dunia umeanza kufunguka kwa wasanii wa Kitanzania.

 

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia mafuta na gesi asilia, Dkt. James Mataragio,akisisitiza jambo kwa watumishi wa EWURA alipotembelea banda la EWURA  katika  maonesho ya Wiki ya Nishati 2026 yanayoendelea katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia mafuta na gesi asilia, Dkt. James Mataragio, amewaomba waheshimiwa wabunge na wadau mbalimbali kuendelea kutembelea maonesho ya Wiki ya Nishati 2026 yanayoendelea katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma, ili kupata elimu juu ya shughuli za kimkakati zinazotekelezwa na taasisi zilizo chini ya wizara hiyo pamoja na kubaini fursa za uwekezaji zinazopatikana.

Akiwa akiwa katika banda la Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), Dkt. Mataragio amesema mamlaka hiyo imeendelea kuwa nguzo muhimu katika kuhakikisha uwiano kati ya maslahi ya watoa huduma na watumiaji wa huduma zinazodhibitiwa, ikiwemo mafuta, gesi asilia na umeme.

“Tumeshuhudia jitihada kubwa zinazofanywa na EWURA katika kusimamia ubora wa huduma na bei stahiki, jambo ambalo linachangia kukuza uchumi na kulinda wananchi,” amesema Dkt. Mataragio.

Ameongeza kuwa uwepo wa EWURA katika maonesho hayo unatoa fursa kwa wananchi kupata elimu kuhusu haki na wajibu wao katika matumizi ya nishati, sambamba na kuelewa mifumo ya udhibiti inayolenga kuboresha huduma na fursa mbalimbali za uwekezaji.

Kwa upande wao, baadhi ya wabunge waliotembelea banda hilo pia waliipongeza EWURA kwa uwajibikaji wake, wakisema imekuwa mstari wa mbele kusikiliza na kushughulikia changamoto zinazowakabili wananchi katika sekta ya nishati pamoja na kuhakilisha upatikanaji wa huduma bora kwa wananchi.

Wiki ya Nishati 2026 imewakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya nishati, zikiwemo taasisi zote zilizo chini ya Wizara ya Nishati kwa lengo la kuonesha maendeleo na fursa zilizopo katika sekta hiyo muhimu kwa ustawi wa uchumi wa taifa.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia mafuta na gesi asilia, Dkt. James Mataragio,akipata maelezo kutoka kwa Kaimu Meneja wa Mawasiliano na Uhusiano wa EWURA, Bw.Wilfred Mwakalosi,alipotembelea banda la EWURA  katika  maonesho ya Wiki ya Nishati 2026 yanayoendelea katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia mafuta na gesi asilia, Dkt. James Mataragio,akipata maelezo kutoka kwa Kaimu Meneja wa Mawasiliano na Uhusiano wa EWURA, Bw.Wilfred Mwakalosi,alipotembelea banda la EWURA  katika  maonesho ya Wiki ya Nishati 2026 yanayoendelea katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia mafuta na gesi asilia, Dkt. James Mataragio,akisisitiza jambo kwa watumishi wa EWURA alipotembelea banda la EWURA  katika  maonesho ya Wiki ya Nishati 2026 yanayoendelea katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi, Dkt. James Mataragio akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kutembelea Banda la EWURA kwenye Maonesho ya Wiki ya Nishati 2026 yanayoendelea katika Viwanja vya Bunge Jijini Dodoma

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi, Dkt. James Mataragio akipokea zawadi kutoka kwa Kaimu Meneja wa Mawasiliano na Uhusiano wa EWURA, Bw.Wilfred Mwakalosi, mara baada ya kutembelea Banda la EWURA kwenye Maonesho ya Wiki ya Nishati 2026 yanayoendelea katika Viwanja vya Bunge Jijini Dodoma

Wabunge mbalimbali wakipata elimu walipotembelea banda la EWURA  katika  maonesho ya Wiki ya Nishati 2026 yanayoendelea katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia mafuta na gesi asilia, Dkt. James Mataragio,akizungumza mara baada ya kutembelea mabanda ya taasisi zilizo chini ya Wizara ya Nishati  katika  maonesho ya Wiki ya Nishati 2026 yanayoendelea katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma.


Na Karama Kenyunko - Michuzi Tv.

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amezielekeza wizara tano muhimu kuchukua hatua za haraka kuimarisha ustawi wa mama na baba lishe, akiwatambua kama mhimili muhimu wa uchumi.

Akizungumza leo Aprili 21, 2026 katika Kongamano la Kitaifa la Mama na Baba lishe lililofanyika Dar es Salaam, Rais almeagiza Wizara za Fedha, Afya, Nishati, Maendeleo ya Jamii (Wanawake, Jinsia, Wazee na Makundi Maalum), pamoja na Habari na TEHAMA, na Ofisi ya Waziri Mkuu–Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), kushirikiana kuboresha mazingira ya kazi, heshima na ulinzi kwa wafanyabiashara hao.

Ameisema mama na baba lishe ni nguzo muhimu ya ajira na uchumi wa maeneo ya mijini na vijijini, hivyo wanapaswa kuheshimiwa na kulindwa dhidi ya manyanyaso.

Rais ameelekeza Wizara ya Maendeleo ya Jamii kushirikiana na taasisi za kifedha kupanua mikopo na mafunzo kwa wafanyabiashara hao, huku TAMISEMI ikitakiwa kuhakikisha upatikanaji wa maeneo rasmi ya kufanyia biashara yenye miundombinu rafiki.

Aidha, Wizara ya Afya imeagizwa kuboresha upatikanaji wa huduma za afya, wakati Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) ukitakiwa kuongeza uhamasishaji wa uandikishaji wa wanachama.

Wizara ya Fedha imehimizwa kuimarisha huduma za kifedha zinazolengwa kwa makundi haya pamoja na kujenga uwezo wao, huku Wizara ya Nishati ikitakiwa kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Rais pia amesisitiza umuhimu wa kuanzishwa kwa vituo vya malezi ya watoto (daycare) ili kusaidia wazazi wanaofanya biashara hizo.

Alithibitisha dhamira ya serikali kushirikiana na sekta binafsi ili kuirasimisha sekta hii na kuifanya kuwa mchangiaji rasmi na endelevu wa uchumi.

Ameeleza kuwa mageuzi hayo ni sehemu ya ajenda pana ya serikali ya kuimarisha maisha ya sekta isiyo rasmi, kuboresha mazingira ya kazi mijini, na kuhakikisha ukuaji wa uchumi jumuishi usiomwacha mtu nyuma.

Kwa upande wake, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Wanawake, Jinsia, Wazee na Makundi Maalum, Dorothy Gwajima, amesema mama na baba lishe ni nguvu kubwa katika uchumi usio rasmi, wakichangia ajira na kipato kwa wananchi wengi.

Amesema tayari juhudi zinaendelea kuboresha utambuzi wa wafanyabiashara hao, kupanua matumizi ya nishati safi ya kupikia, na kuimarisha ushirikiano kati ya serikali, sekta binafsi na vyama vyao nchi nzima.

Katibu wa Chama cha Wauza Chakula (UMALITA), Havijawa Omary, amesema kongamano hilo linaashiria mwanzo mpya wa ujumuishaji na heshima kwa wafanyabiashara hao.

Ameupongeza uongozi wa Rais Samia, akimtaja kama kiongozi wa mabadiliko. Aliongeza kuwa UMALITA, kilichoanzishwa mwaka 2002, kina wanachama 5,000 kwa sasa na kinatarajia kufikia 100,000 ifikapo mwaka 2030. Pia alibainisha kuwa programu ya simu (App) ya UMALITA itarahisisha upatikanaji wa mikopo na urasimishaji wa biashara, licha ya changamoto za mitaji na masharti ya mikopo.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, alisema wafanyabiashara hao wanaendelea kupata heshima kutokana na mageuzi yanayoendelea pamoja na matumizi ya nishati safi.

Alisema pia maelekezo ya matumizi ya nishati safi yameanza kutekelezwa hata mashuleni, ambapo takribani shule 300 tayari zinatumia gesi ya kupikia.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Dkt. John Jingu, amesema kongamano hilo la kwanza la kitaifa limewaleta pamoja wafanyabiashara hao kujifunza na kupanga mustakabali wa sekta hiyo.

Kaulimbiu ya kongamano hilo ilikuwa kulinda amani na umoja, ikisisitiza kuwa amani ni hazina ya pamoja kwa wafanyabiashara, na ni msingi wa maendeleo ya taifa na uchumi jumuishi.

Kwa ujumla, kongamano hilo limeelezwa kuwa hatua muhimu katika kuirasimisha sekta ya wauza chakula, kukuza heshima, ujumuishaji na fursa za kiuchumi kwa maelfu ya wafanyabiashara wadogo nchini.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimkabidhi Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Profesa Riziki Shemdoe mfano wa hundi ya Shilingi bilioni 94.158,250,400/= kwa ajili ya mikopo ya Wanawake, Vijana na Watu wenye Ulemavu kwenye Kongamano la Kitaifa la Mama na Baba lishe, lililofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Jijini Dar es Salaam, tarehe 21 Aprili, 2026


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Tuzo ya Heshima ya Malkia wa Nishati safi kutoka kwa Mwenyekiti wa Umoja wa Mama na Baba Lishe Tanzania (UMALITA) Bi. Havijawa Omary katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Jijini Dar es Salaam, tarehe 21 Aprili, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akihutubia kwenye Kongamano la Kitaifa la Mama na Baba Lishe Tanzania (UMALITA) lililofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Jijini Dar es Salaam, tarehe 21 Aprili, 2026


Top News