Na Mwandishi Wetu

MAMLAKA ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) imeipongeza Sanlam Allianz kwa kuanzisha Mfuko mpya wa 'USD Fixed Income Fund' utakaowawezesha wawekezaji na wananchi kuweka akiba ya fedha za kigeni (sola ya Marekani).

Akizungumza kwenye hafla ya uzinduzi wa Mfuko huo mwishoni mwa wiki, Mkurugenzi wa Usimamizi wa Masoko na Uchunguzi wa CMSA, Exaut Julius, alisema mfuko huo utachochea uchumi wa nchi na kuongeza akiba ya fedha za kigeni kwenye mzunguko.

"Tunawapongeza kwa kuzinduaa Mfuko huu kwa wakati muafaka kwani utachangia maendeleo yamasoko ya mitaji hapa nchini," alisema Julius.

Aidha, alisema Mfuko huo unaonyesha ushirikiano mzuri kati ya CMSA na wadau wake katika kukuza masoko endelevu na mitaji.

"Upatikanaji wa bidhaa bora za uwekezaji zinazoendana na viwango vya kimataifa ni nguzo muhimu katika kupanua ushiriki wa wawekezaji na kuendeleza masoko na mitaji hapa nchini," alisema Julius.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Muu wa kampuni hiyo, Jonathan Stichbury, alisema kuanzishwa mfuko huo ni hatua muhimu katika kuhamasisha utamaduni wa uwekezaji wenye tahadhari na kupanua fursa za uwekezaji zinazotumia dola ya marekani nchini Tanzania.

Alisisitiza pia dhamira yao katika kuzingatia uwazi, kufuata sheria na kanuni, pamoja na kuleta thamani ya muda mrefu kwa wawekezaji wote.

 

*Sekta ya mafuta na gesi kama nguzo ya maendeleo ya Taifa*

Na Rashid Mtagaluka.

Tarehe 14 Novemba 2025, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, aliwasilisha hotuba yake ya kwanza ya muhula mpya mbele ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hotuba iliyobeba maelekezo ya kimkakati kuhusu mwelekeo wa Serikali katika kusimamia uchumi na rasilimali za Taifa.

Katika hotuba hiyo, Rais aliweka bayana dhamira ya Serikali ya kutumia ipasavyo rasilimali zilizopo, hususan mafuta na gesi asilia, kama chachu ya maendeleo ya viwanda, ukuaji wa uchumi na ustawi wa wananchi. Alisisitiza kuwa rasilimali hizo ni mhimili muhimu wa safari ya Taifa kuelekea maendeleo endelevu.

Ndani ya siku 100 za mwanzo wa muhula huo, sekta ya mafuta na gesi imeendelea kujitokeza kama moja ya nguzo kuu za utekelezaji wa dira hiyo, chini ya uangalizi wa Serikali kupitia Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC).

Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizojaaliwa akiba kubwa ya gesi asilia, rasilimali ambayo ina uwezo mkubwa wa kubadili taswira ya uchumi wa Taifa endapo itasimamiwa kwa weledi, uwazi na uwajibikaji. Akihutubia Bunge, Rais Samia alisisitiza kuwa rasilimali hizi ni mali ya wananchi wote, hivyo matumizi yake lazima yaongozwe na maslahi ya Taifa kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

Katika muktadha huo, TPDC imeendelea kutekeleza majukumu yake ya kisheria na kikatiba kama wakala wa Serikali katika sekta ya mafuta na gesi, kwa kuzingatia kikamilifu maelekezo na dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita.

Katika siku 100 za mwanzo wa muhula mpya wa Rais Samia, juhudi zimeelekezwa katika kuimarisha usimamizi wa rasilimali za gesi asilia, kusimamia mikataba ya utafutaji na uzalishaji, kuimarisha ushirikiano na wawekezaji, pamoja na kuhakikisha kuwa rasilimali hii inaleta manufaa ya moja kwa moja kwa wananchi.

Moja ya maeneo yaliyopata uzito mkubwa katika hotuba ya Rais ni matumizi ya gesi asilia kama nishati safi, nafuu na salama kwa ajili ya viwanda, uzalishaji wa umeme na matumizi ya majumbani. Ndani ya kipindi hiki cha siku 100, Serikali kupitia taasisi zake ikiwemo TPDC, imeendelea kusimamia na kuimarisha miradi ya uzalishaji na usambazaji wa gesi asilia katika maeneo mbalimbali ya nchi.

Hatua hizi zinalenga kupunguza gharama za uzalishaji viwandani, kukuza uchumi wa ndani na kuongeza fursa za ajira kwa Watanzania, sambamba na kupunguza utegemezi wa nishati zisizo rafiki kwa mazingira.

Aidha, Rais Samia alisisitiza umuhimu wa sekta ya mafuta na gesi kuchangia maendeleo ya jamii zinazozunguka maeneo ya uzalishaji. Katika siku 100 hizi, dhana ya Uwajibikaji wa Kampuni kwa Jamii (CSR) imeendelea kupewa kipaumbele katika utekelezaji wa majukumu ya TPDC.

Kupitia miradi ya kijamii katika sekta za elimu, afya, maji na miundombinu, juhudi zimeelekezwa katika kuhakikisha kuwa wananchi wanapata manufaa ya moja kwa moja ya uwepo wa rasilimali hizi katika maeneo yao.

Katika hotuba yake, Rais Samia aligusia pia umuhimu wa kujenga uwezo wa Watanzania kushiriki kikamilifu katika sekta ya mafuta na gesi. Ndani ya siku 100, jitihada zimeendelea kuimarisha ushiriki wa wazawa (local content) kwa kutoa fursa kwa wataalamu wa ndani, makampuni ya Kitanzania na vijana wanaosomea masuala ya nishati.

Hatua hii inaakisi dhamira ya Serikali ya kuhakikisha kuwa sekta ya mafuta na gesi haiwanufaishi wawekezaji pekee, bali inakuwa jukwaa la kukuza ajira, ujuzi na teknolojia kwa Watanzania.

Sambamba na hilo, masuala ya ulinzi wa mazingira na usalama yameendelea kupewa uzito unaostahili. 

Akihutubia Bunge, Rais Samia alisisitiza kuwa maendeleo ya kiuchumi hayawezi kupatikana kwa gharama ya mazingira. Ndani ya siku 100, TPDC imeendelea kusimamia shughuli za utafutaji, uzalishaji na usambazaji wa gesi kwa kuzingatia viwango vya kitaifa na kimataifa vya uhifadhi wa mazingira, afya na usalama kazini.

Kwa ujumla, siku 100 za mwanzo wa muhula mpya wa Rais Samia Suluhu Hassan zimeonesha mwelekeo thabiti wa Serikali katika kusimamia sekta ya mafuta na gesi kwa maslahi mapana ya Taifa. 

Kupitia TPDC, Serikali imeendelea kuimarisha misingi ya usimamizi bora wa rasilimali, kuongeza uwazi na kuimarisha mchango wa sekta hii katika uchumi wa Taifa.

Ingawa safari ya maendeleo ya sekta ya mafuta na gesi bado ni ndefu na yenye changamoto, dalili zilizojitokeza ndani ya siku 100 hizi zinaonesha dhamira ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Sita kuhakikisha kuwa rasilimali hii inakuwa baraka kwa Watanzania wote.

Katika kutekeleza maono aliyoyatoa bungeni tarehe 14 Novemba 2025, Rais Samia ameendelea kusisitiza mshikamano kati ya Serikali, taasisi zake, sekta binafsi na wananchi. Sekta ya mafuta na gesi, chini ya usimamizi wa TPDC, inaendelea kubaki kuwa moja ya nguzo muhimu katika safari ya Tanzania kuelekea uchumi wa kati wa juu na maendeleo jumuishi. Siku 100 hizi ni mwanzo tu, lakini ni mwanzo unaobeba matumaini makubwa kwa mustakabali wa Taifa.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Soko Kuu jipya la Kariakoo, Ilala Jijini Dar es Salaam tarehe 08 Februari, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha ya pamoja na Waziri Mkuu Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba mara baada ya kufungua Soko Kuu jipya la Kariakoo, Ilala Jijini Dar es Salaam tarehe 08 Februari, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa mbele ya Soko Kuu jipya la Kariakoo mara baada ya ufunguzi uliofanyika Sokoni hapo, Ilala Jijini Dar es Salaam tarehe 08 Februari, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akivuta kitambaa kuashiria uzinduzi wa Soko Kuu jipya la Kariakoo, Ilala Jijini Dar es Salaam tarehe 08 Februari, 2026.

Wageni mbalimbali wakiwa kwenye hafla ya ufunguzi wa Soko Kuu jipya la Kariakoo, Ilala Jijini Dar es Salaam tarehe 08 Februari, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Waziri Mkuu Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba wakati wa hafla ya ufunguzi wa Soko Kuu jipya la Kariakoo, Ilala Jijini Dar es Salaam tarehe 08 Februari, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye hafla ya uzinduzi wa Soko Kuu jipya la Kariakoo, Ilala Jijini Dar es Salaam tarehe 08 Februari, 2026.

Matukio mbalimbali katika hafla ya ufunguzi wa Soko Kuu jipya la Kariakoo, Ilala Jijini Dar es Salaam tarehe 08 Februari, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea zawadi ya picha mara baada ya kufungua Soko Kuu jipya la Kariakoo, Ilala Jijini Dar es Salaam tarehe 08 Februari, 2026.



Katika kuadhimisha miaka 19 ya kuanzishwa kwa kiwanda cha kuunganisha magari cha GF, uongozi wa kiwanda hicho umesema unajivunia kuwa sehemu ya kuzalisha ajira, huku ukieleza kuwa asilimia 90 ya wafanyakazi wake ni wazawa.

Akizungumza na waandishi wa habari, leo Februari 07, 2026, makao makuu ya kiwanda hicho yaliyopo Kibaha mkoani Pwani, Meneja Mkuu wa kiwanda cha GF, Ezra Mereng, amesema miaka 19 ya dira na matumaini yalianza kama ndoto, lakini hadi sasa kiwanda hicho kinajivunia kuzalisha magari ya aina mbalimbali.

“Leo tunajivunia kusherehekea miaka 19 ya GF, na sisi kama kiwanda tunajivunia kuwa zaidi ya asilimia 90 ya wafanyakazi ni vijana wazawa wa hapa Tanzania waliotoka katika vyuo mbalimbali hapa nchini."

Naye Meneja Chapa na Masoko wa GF Group, Salman Karmal  pamoja na kufurahia mafanikio ya kiwanda hicho, ameishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa kufungua fursa za uwekezaji zinazowavutia wawekezaji wengi kuja kuwekeza nchini.

Amesema katika kuadhimisha miaka 19 ya GF, kiwanda hicho kimekuja na mpango wa kurudisha kwa jamii, ambapo wameanza kwa kutembelea watu wenye mahitaji maalumu pamoja na kufadhili timu ya mpira wa miguu ya Nyumbu FC iliyopo jirani na kiwanda hicho, ambayo imekuwa ikifanya vizuri kwenye michezo yake mbalimbali.

“Tunaishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuweza kufungua milango rafiki ya uwekezaji inayotufanya tuwe na uthubutu wa kujiimarisha zaidi katika maeneo mbalimbali ya kibiashara".

Kwa upande wake, Sefroza Mwizarubi, ambae ni mnufaika wa program ya kuchukua wanafunzi vyuoni , amewashukuru viongozi wa GF kwa kutoa nafasi kwa wahitimu wa vyuo mbalimbali kwenda kujifunza namna ya kuunganisha magari, jambo linalowafanya kuwa wabobezi katika nyanja hiyo.

“Mimi ni mnufaika wa mpango wa GF wa kuchukua wanafunzi kutoka vyuoni kwa ajili ya kuja kupata ujuzi wa kuunganisha magari, lakini pia kupata ajira,” amesema Mwizarubi.
Meneja Mkuu wa kiwanda cha GF Vehicle Assemblers,  Ezra Mereng akizuingumza na wafanyakkazi wa kiwanda hicho wakati wa hafla ya madhimisho ya miaka 19 ya kampuni ya GF mkoani Pwani





Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza, Bw. Balandya Elikana,akizungumza wakati akifungua mafunzo ya kuwajengea uwezo wafanyabiashara jijini Mwanza,ili  kuwaongezea uelewa kuhusu masuala ya ushindani wa soko pamoja na taratibu za kupata haki katika shughuli za kibiashara yaliyoandaliwa na Baraza la Ushindani wa Soko (FCT).

Na.Mwandishi Wetu-MWANZA

 BARAZA  la Ushindani wa Soko (FCT)  limetoa mafunzo ya kuwajengea uwezo wafanyabiashara jijini Mwanza, yakilenga kuwaongezea uelewa kuhusu masuala ya ushindani wa soko pamoja na taratibu za kupata haki katika shughuli za kibiashara.

Mafunzo hayo yaliwakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya biashara, ambapo waliipongeza Wizara ya Viwanda na Biashara chini ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa juhudi zake za kuweka mazingira bora ya biashara na uwekezaji kupitia uwepo wa chombo huru cha kusimamia na kudhibiti ushindani wa soko.

Akifungua semina hiyo, Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza, Bw. Balandya Elikana, alisema kuwa mafunzo hayo ni muhimu kwa wadau wa sekta ya biashara kwani yanawawezesha kuelewa kwa kina majukumu ya Baraza la Ushindani pamoja na umuhimu wa mshikamano katika utekelezaji wa sheria za ushindani.

“Kupitia semina hii, wadau watapata uelewa mpana kuhusu Baraza la Ushindani na nafasi yake katika kulinda haki za mlaji pamoja na kuendeleza ushindani wa haki katika soko.”Alisema Bw.Elikana

Akizungumza katika mafunzo hayo, Msajili wa Baraza la Ushindani, Bw. Mbegu Kaskasi, alisema kuwa Baraza lipo kwa ajili ya kulinda masuala yote yanayohusu ushindani wa soko na kuchochea maendeleo ya kiuchumi nchini. Alieleza kuwa utekelezaji wa majukumu ya Baraza unalenga kuimarisha misingi ya utawala bora kwa kuhakikisha sheria za ushindani zinatekelezwa kikamilifu, kwa haki na kwa uwazi.

Aidha, aliongeza kuwa Baraza huhakikisha mamlaka za udhibiti zinazingatia taratibu na kanuni za ushindani wakati wa utekelezaji wa majukumu yao, sambamba na kutoa majibu sahihi na ya haraka katika migogoro ya kibiashara. Alibainisha kuwa hatua hiyo inalenga kumlinda mlaji dhidi ya vitendo vinavyodhoofisha ushindani, hivyo kuchangia katika ujenzi wa uchumi shindani, jumuishi na wenye tija kwa Watanzania.

Kwa upande wake, Meneja wa Mkoa wa Chemba ya Wafanyabiashara, Bw. Hassan Karambi, alisema kuwa amepata elimu yenye manufaa makubwa kupitia programu ya Baraza ya kuwajengea uwezo wadau.

Alieleza kuwa mafunzo hayo yamewasaidia wafanyabiashara kufahamu kuwa endapo hawataridhika na maamuzi ya mamlaka za udhibiti kama LATRA, TCRA, TCAA, EWURA, PURA pamoja na Tume ya Ushindani (FCC), wana haki ya kukata rufaa katika Baraza la Ushindani ili kupata haki yao.

Naye Meneja wa Mamlaka ya Mawasiliano Kanda ya Ziwa, Bi. Imelda Salumu, alifafanua utaratibu wa Baraza katika kupokea rufaa kutoka kwa wadau.

Alisema kuwa malalamiko huanza kwa mtoa huduma husika, na endapo hayatapatiwa ufumbuzi, hufikishwa katika mamlaka ya udhibiti kama hatua ya kwanza ya rufaa. Aliongeza kuwa iwapo mlalamikaji hataridhishwa na maamuzi ya mamlaka hiyo, utaratibu humruhusu kuwasilisha rufaa katika Baraza la Ushindani kwa hatua zaidi za kisheria.



Na Mwandishi Wetu, Manyara.

SERIKALI imeanza utekelezaji wa mradi mkubwa wa kusambaza umeme katika vitongoji 267 vya Mkoa wa Manyara kwa gharama ya Shilingi bilioni 45.8 kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA), ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya umeme na kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.


Akizungumza wakati wa hafla ya kumtambulisha mkandarasi wa mradi huo, mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Herini Mhina, amesema mkataba wa utekelezaji wa mradi huo ni wa miaka mitatu na utatekelezwa katika halmashauri zote za Mkoa wa Manyara.



Mhandisi Mhina amesema mradi huo unalenga kufikisha huduma ya umeme katika vitongoji ambavyo bado havijafikiwa, hatua itakayosaidia kuboresha maisha ya wananchi, kukuza shughuli za kiuchumi pamoja na kuimarisha upatikanaji wa huduma za kijamii kama afya na elimu.


Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, amewaagiza Wakuu wa Wilaya zote za mkoa huo kutoa ushirikiano wa karibu kwa mkandarasi ili kuhakikisha mradi unatekelezwa kwa wakati na kwa viwango vinavyotakiwa.


Mhe. Sendiga pia amesisitiza umuhimu wa viongozi kutoa elimu kwa wananchi kuhusu utekelezaji wa mradi huo, akieleza kuwa mradi wa kusambaza umeme hauna fidia, hivyo ni muhimu wananchi kuelewa taratibu zake ili kuepusha changamoto zisizo za lazima.



Naye mkandarasi aliyekabidhiwa utekelezaji wa mradi huo, Bw. Patrick Mong, amesema lengo lao ni kuukamilisha mradi huo ndani ya miezi 33, huku akibainisha kuwa kazi za utekelezaji zinaanza rasmi Februari 9 mwaka huu.

Amesema mkandarasi amejiandaa kikamilifu kuhakikisha mradi unakamilika kwa ubora na kwa muda uliopangwa ili wananchi wa Mkoa wa Manyara wanufaike na huduma ya umeme kwa maendeleo endelevu.

Na Kassim Nyaki, Ngorongoro.

Mabadiliko makubwa katika ushirikishwaji wadau wa sekta ya utalii yameibuliwa na uongozi Mamlaka ya Hifadhi ya  Ngorongoro ikianza mwanzo wa safari mpya ya simulizi kwa chapa ya Destination Ngorongoro kwa kuzungumza sauti moja, iliyo thabiti, yenye kujiamini na kukumbukwa.

Ngorongoro imeamua kuzindua shindano la upigaji  picha kwa waongoza watalii (Tour Guides)  lijulikanalo kama “The Birth of Wonders photo competition” katika eneo la Ndutu hususan msimu huu wa mazalia ya Nyumbu.

Akitangaza kampeni hiyo Kamishna Msaidizi Mwandamizi anayesimamia huduma za Utalii na Masoko Mariam Kobelo ameeleza kuwa shindano hilo linahusu eneo la Ndutu ambapo ndipo Safari Kuu ya Nyumbu huzaliwa na maisha kuanza ambapo eneo hilo hadithi ya Ngorongoro hujirudia upya kila mwaka.

“Waongoza Watalii ni mabalozi wetu muhimu katika kuisimulia Ngorongoro kwa dunia, katika msimu huu wa uzaaji wa nyumbu hapa Ndutu, tunawaalika kutumia lenzi zao kunasa pumzi za kwanza za uhai wa ndama, hatua za kwanza za ndama, mahusiano ya mama na mwana, 

Waongoza watalii watapaswa kupiga picha na kuzituma kupitia akaunti zao za instagram, _tag_ na kushiriki (collaborate) na akaunti rasmi ya  _instagram_ ya ngorongoro ijulikanayo kama (@visitngorongoro

Katika shindano hilo  la upigaji picha ( _The Birth of Wonders photo competition)_ Washindi watachaguliwa kwa kuzingatia ushiriki (engagement) wa watazamaji pamoja na kufuata masharti yote ya shindano ambapo mshindi wa kwanza atajinyakulia kitita kinono cha shilingi Milioni  3,000,000, mshindi wa pili shilingi milioni 2,000,000 na mshindi wa tatu atajishindia shilingi milioni 1,000,000 mtawalia.

Waongoza Watalii ambao ni washiriki wa kampeni hii wanakuwa wasimulizi wa sauti ya chapa ya _Destination Ngorongoro_ Kwani wao ndiyo mashuhuda wa kwanza wa simulizi ya uzao wa nyumbu.









 


Top News