Na Mwandishi Wetu,Kahama

WCHIMBAJI  wadogo wa Dhahabu katikà kijiji cha Bukooba, Manispaa ya Kahama, mkoa wa Shinyanga, wameiomba Serikali kupelekewa huduma ya umeme na maji ili kurahisisha shughuli zao. 

Wachimbaji hao wametoa maombi hayo mbele ya waandishi wa vyombo mbalimbali waliokwenda katikà mgodi huo kwa lengo la kujionea shughuli za uchimbaji Madini. 

"Kwenye mgodi wetu huu wa Bukooba tunazo changamoto mbili kubwa. Kwanza hatuna umeme wa kuendeshea mitambo yetu ya uchimbaji na uchenjuaji, badala yake tunatumia dizeli na petroli hali ambayo inatuongezea gharama za uzalishaji ikizingatiwa Hali ya sasa ya bei za mafuta ambayo ipo juu", alieleza Mkurugenzi Mkuu wa mgodi huo Said Ibrahim Kapesya. 

Aliongeza kuwa, "Pia tunayo changamoto nyingine ya ukosefu wa maji kwenye mgodi wetu kwa ajili ya kuchenjulia dhahabu. Hali hii inatusababishia usumbufu na gharama kubwa za uzalishaji kwasababu tunafuata maji umbali mrefu kutoka hapa, tunaiomba serikali ya mama yetu Rais Samia Suluhu Hassan itusogezee huduma hizi muhimu ili kurahisisha na kuboresha shughuli zetu", alibainisha Kapesya.

Kapesya aliishukuru serikali kwa kuwapatia leseni ya utafiti na uchimbaji katikà kijiji cha Bukooba bila kujali hali zao za kiuchumi, huku akimuomba waziri wa madini kutokimbilia kufuta leseni za wachimbaji wenye uwezo mdogo wa fedha bali awavumilie kwani wachimbaji hao wanaisaidia serikali kupunguza idadi ya vijana wasiokuwa na kazi mitaani.

" Kwa mfano, leseni yetu hii inawanufaisha zaidi ya watanzania 500 kwa kuwawezesha kujiajiri, na wengi kati ya watu hao ni vijana na Wanawake", alifafanua mkurugenzi huyo.

Aidha, Kapesya ameiomba serikali kuwasaidia wachimbaji wadogo kupata mikopo ya fedha kutoka taasisi za fedha nchini  ambayo itawawezesha kununua vifaa vya kisasa vya upimaji na uchimbaji madini ili waweze kufanya kazi zao kwa uhakika na ufanisi. 







Na Janeth Raphael MichuziTv 

Wizara ya Maliasili na Utalii, kupitia Mfuko wa Uhifadhi wa Wanyamapori Tanzania (TWPF), imeandaa Rasimu ya Mwongozo wa Uanzishaji na Usimamizi wa Maeneo ya Jumuiya za Hifadhi za Wanyamapori (Wildlife Management Areas – WMAs), ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali kuimarisha usimamizi wa maeneo hayo na kutatua changamoto zinazokabili jumuiya zinazoyasimamia.

Akifungua kikao kazi shirikishi cha kuandaa rasimu hiyo jijini Dodoma kwa niaba ya Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori, Mkurugenzi Msaidizi wa Idara hiyo, Bi. Kay Kagaruki, alisema hatua hiyo inatekeleza maelekezo ya Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji, ya kuboresha mfumo wa usimamizi wa uhifadhi kwa kushirikiana na jamii kupitia WMAs.

Amesema Serikali imeendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa uhifadhi kuhakikisha maeneo hayo yanaendeshwa kwa ufanisi zaidi kupitia maboresho ya sera, miongozo na mifumo ya usimamizi inayolenga kuongeza manufaa kwa wananchi na kulinda rasilimali za wanyamapori.

"Serikali kupitia Wizara kwa kushirikiana na wadau wa uhifadhi imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha jumuiya za hifadhi kwa kutatua changamoto zinazozikabili na kuhakikisha zinafanya kazi kwa ufanisi zaidi," alisema Bi. Kagaruki.

Aidha, amewataka wananchi kuendelea kushiriki kikamilifu katika shughuli za uhifadhi, akisisitiza kuwa kulinda maliasili ni wajibu wa kila Mtanzania kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Kwa upande wake, Mratibu wa kikao hicho, Rose Mndendemi, alisema hadi sasa Tanzania ina jumla ya Maeneo ya Jumuiya za Hifadhi za Wanyamapori (WMAs) 24 yaliyopata idhini na haki ya matumizi ya rasilimali za wanyamapori, huku jumuiya nyingine 16 zikiwa katika hatua mbalimbali za kukamilisha taratibu za kupata haki hiyo.

Naye Afisa Wanyamapori wa Halmashauri ya Wilaya ya Babati,  Christopher Laizer, ameipongeza Wizara kwa kuwashirikisha wadau katika kuandaa rasimu ya mwongozo huo, akisema utakapokamilika utasaidia kuongeza ufanisi katika usimamizi wa WMAs na kuimarisha mchango wake katika maendeleo ya wananchi na uhifadhi endelevu wa rasilimali za taifa.

Kikao kazi hicho cha siku tatu kinawakutanisha maafisa kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii, Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), Maafisa Wanyamapori wa Wilaya, viongozi wa Jumuiya za Hifadhi za Wanyamapori pamoja na wadau mbalimbali wa sekta ya uhifadhi, kwa lengo la kukamilisha mwongozo utakaoboresha uanzishaji na usimamizi wa WMAs nchini.










Na Karama Kenyunko Michuzi Tv
IDARA ya Uchumi na Utalii ya Dubai (DET) imefanya mkutano wake wa kila mwaka wa biashara ya utalii jijini Dar es Salaam, ukiwakutanisha mawakala 130 wa safari, waendeshaji wa utalii, mashirika ya ndege na wadau wa sekta ya utalii kwa lengo la kuimarisha ushirikiano na sekta ya usafiri nchini Tanzania pamoja na kutangaza vivutio vipya vinavyopatikana kwa watalii wanaotembelea Dubai.

Mkutano huo ni sehemu ya mkakati wa DET wa kuendelea kushirikiana na soko la Afrika Mashariki, ambalo linaendelea kukua kwa kasi katika safari za kimataifa.

Kwa mujibu wa DET, Tanzania ni miongoni mwa masoko muhimu ya utalii barani Afrika kutokana na kuongezeka kwa mahitaji ya safari za kimataifa, mahusiano mazuri ya kibiashara pamoja na uwepo wa safari nyingi za moja kwa moja za ndege kati ya Tanzania na Dubai.

Takwimu za DET zinaonesha kuwa mwaka 2025 bara la Afrika lilichangia takribani wageni 897,000 waliotembelea Dubai, sawa na asilimia tano ya wageni wote wa kimataifa waliofika jijini humo, huku Tanzania ikiendelea kuwa miongoni mwa nchi zinazochangia ongezeko hilo.

Wasafiri kutoka Tanzania pia wananufaika na safari 33 za moja kwa moja kila wiki kutoka Dar es Salaam na Zanzibar kwenda Dubai, hali inayoufanya mji huo kuwa miongoni mwa maeneo rahisi kufikika kwa wasafiri wa Tanzania.

DET imeeleza kuwa Watanzania wengi sasa wanapendelea kutembelea maeneo yanayotoa huduma nafuu, burudani za familia, ununuzi, utamaduni na vivutio mbalimbali katika eneo moja.

Akizungumza wakati wa mkutano huo, Meneja Msaidizi wa Operesheni za Kimataifa wa Dubai Corporation for Tourism and Commerce Marketing (DCTCM), Khalaf Alaleeli, alisema mkutano huo unadhihirisha dhamira ya Dubai ya kuendelea kuimarisha ushirikiano na sekta ya usafiri nchini Tanzania.

Alisema Dubai inaendelea kuwakaribisha wageni kwa kutoa huduma zenye thamani kubwa, vivutio vya kiwango cha kimataifa na uzoefu unaokidhi mahitaji ya kila aina ya msafiri, wakiwemo familia, wasafiri binafsi, makundi pamoja na wasafiri wa kibiashara.

Kwa mujibu wa DET, Dubai imeendelea kupanua huduma zake za utalii kwa kuongeza malazi yenye gharama nafuu, vivutio vya bure na vya gharama ndogo, maeneo mapya ya burudani kwa familia pamoja na moja ya miji yenye migahawa mingi na tofauti zaidi duniani, ikiwa na zaidi ya migahawa 13,000.

Aidha, Dubai imekuwa jiji la kwanza katika Ukanda wa Mashariki wa Dunia kutambuliwa kama Certified Autism Destination, hatua inayodhihirisha dhamira yake ya kuhakikisha utalii unakuwa jumuishi na unaowafaa watu wenye mahitaji maalumu.

DET imeeleza pia kuwa Dubai inaendelea kuwa miongoni mwa miji salama zaidi duniani kwa watalii, huku miundombinu ya utalii, hoteli, vivutio na huduma za umma zikiendelea kufanya kazi kwa kawaida.






Na Mwandishi Wetu
BARAZA la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET) limewataka wazazi na walezi kuhakikisha wanapata taarifa sahihi kuhusu usajili wa vyuo na kozi zinazotolewa kabla ya kuwaandikisha watoto wao, ili kuepusha hasara inayotokana na kusomea kozi zisizotambuliwa na Baraza.

Hayo ameyasema Afisa Uthibiti Ubora Mkuu wa NACTVET, Bi. Deborah Ngalemwa, alipokuwa akizungumza na wananchi waliotembelea banda la Baraza hilo katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Bi. Deborah amesema NACTVET imekuwa ikipokea malalamiko kutoka kwa vijana wanaomaliza masomo yao katika baadhi ya vyuo, moja ya malalamiko hayo ikiwa ni pamoja na kutotambulika kwa vyuo na kozi walizosoma. Vijana wengi wamekutana na changamoto hii pale walipotaka kuendelea na masomo au wanapotafuta ajira.

Alieleza kuwa changamoto nyingine ni baadhi ya vyuo kuwaandikisha wanafunzi katika kozi ambazo hawana sifa za kujiunga nazo kulingana na matokeo ya mtihani wa Kidato cha nne, jambo ambalo huwasababishia matatizo wanapohitaji kutambuliwa na mamlaka zingine hasa zile za kitaaluma baada ya kuhitimu.

Aidha, alisema zipo pia kesi za wanafunzi wanaopelekwa kusoma katika vyuo vya nje ya nchi, lakini wanaporejea Tanzania wanashindwa kutambuliwa kwa sababu vyuo walivyosoma havitambuliwi au programu walizosoma hazikukidhi vigezo vilivyowekwa na Baraza.

Bi. Deborah aliwasihi wazazi, walezi na wanafunzi kufika NACTVET au kuwasiliana na Baraza hilo kupitia njia mbalimbali za mawasiliano kabla ya kufanya uamuzi wa kujiunga na chuo chochote, ili kuthibitisha usajili wa Chuo pamoja na uhalali wa kozi wanazokusudia kusoma.

"Baraza limekuwa likipokea malalamiko kutoka kwa vijana wanaoambiwa vyuo walivyosoma havina sifa, ilhali wao na wazazi walikuwa tayari wamegharimia masomo, hali ambayo husababisha usumbufu na hasara kubwa kwa jamii ambayo ingeweza kuepukika kwa kupata ushauri mapema," alisema Bi. Deborah.

Aliongeza kuwa ushauri wa mapema kutoka NACTVET utawasaidia wazazi na wanafunzi kufanya maamuzi sahihi, kulinda uwekezaji wao katika elimu na kuhakikisha wahitimu wanapata sifa zinazotambulika katika soko la ajira na kwa maendeleo ya taaluma zao.

Baraza linaendelea kutoa Elimu kwa jamii kuhusu Umuhimu wa kujua uhalali wa Chuo na kozi kabla kuanza masomo kupitia kampeni zake mbalimbali zinazopatikana kwenye mitandao ya kijamii.
Na Janeth Raphael MichuziTv

Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) kwa kushirikiana na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) zimeandika historia baada ya kufanikisha kwa mara ya kwanza upasuaji wa kuziba matundu ya moyo kwa watoto kutoka nchini Burundi, hatua inayotajwa kuwa mafanikio makubwa katika kuimarisha huduma za kibingwa na kukuza tiba utalii nchini Tanzania.

Mafanikio hayo yametangazwa na Mkurugenzi wa Hospitali ya Benjamin Mkapa, Prof. Abel Makubi, wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma ambapo amesema ushirikiano kati ya BMH na JKCI unaendelea kuzaa matokeo chanya na utaimarishwa zaidi ili kuongeza wigo wa huduma za kibingwa na ubingwa bobezi kwa Watanzania pamoja na wagonjwa kutoka mataifa jirani.

Prof. Makubi amesema hatua hiyo ni ya kihistoria kwa kuwa ndiyo mara ya kwanza kwa taasisi hizo mbili kushirikiana kuwafanyia watoto kutoka nje ya Tanzania upasuaji wa moyo, jambo linaloonesha uwezo wa nchi katika kutoa huduma za matibabu zinazokidhi viwango vya kimataifa.

Amesema Tanzania imejipanga kuhakikisha wagonjwa kutoka ndani na nje ya mipaka yake wanapata huduma bora za kibingwa bila kulazimika kusafiri kwenda mataifa ya mbali kutafuta matibabu yanayopatikana hapa nchini.

"Kwa miaka mingi tumekuwa tukishuhudia wagonjwa wakisafiri kwenda nje kwa huduma ambazo sasa zinaweza kutolewa nchini kwa ufanisi na kwa gharama nafuu zaidi. Dhamira yetu ni kuona Tanzania inakuwa kitovu cha huduma za matibabu kwa ukanda wa Afrika Mashariki na kwingineko," amesema Prof. Makubi.

Akizungumzia hali za wagonjwa hao, Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Moyo na Kifua, Dk. Ahmed Toure, amesema watoto waliopatiwa matibabu walizaliwa na matatizo ya kimaumbile ya moyo yaliyokuwa yakihitaji upasuaji maalumu ili kurekebisha mfumo wa mzunguko wa damu.

Amefafanua kuwa baadhi ya watoto wenye matatizo hayo huzaliwa na hitilafu kwenye mishipa ya moyo inayosababisha damu kutosambaa ipasavyo kwenda kwenye mapafu na sehemu nyingine za mwili, hali ambayo inaweza kusababisha madhara makubwa endapo matibabu hayatatolewa mapema.

Kwa mujibu wa Dk. Toure, watoto wengi huanza kuonesha athari kubwa wanapofikisha umri wa miezi sita hadi mwaka mmoja, hivyo uchunguzi wa mapema na upasuaji kwa wakati ni muhimu katika kuongeza nafasi ya kuishi maisha marefu na yenye afya.

Naye Mratibu wa Tiba Utalii Tanzania, Dk. Asha Mahita, amesema mafanikio hayo yanaendana na malengo ya Serikali kupitia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambayo inalenga kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha huduma za tiba utalii katika ukanda wa Afrika.

Amesema kuwapokea na kuwatibu wagonjwa kutoka Burundi ni ushahidi kuwa uwezo wa wataalamu wa afya nchini unaendelea kuimarika na kwamba huduma zinazotolewa sasa zinavutia wagonjwa kutoka mataifa mengine.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuhakikisha wagonjwa wanaendelea kufuatiliwa baada ya upasuaji ili kuhakikisha wanapata nafuu kamili na kuendelea kuishi maisha yenye afya.

Kwa upande wake, Daktari Bingwa Mbobezi wa Upasuaji wa Moyo kwa Watoto kutoka JKCI, Dk. Godwin Godfrey, amesema ushirikiano kati ya taasisi hizo mbili umeongeza uwezo wa wataalamu kubadilishana uzoefu na kuendelea kuboresha huduma za kibingwa nchini.

Ameeleza kuwa ushirikiano huo unachangia kuwafikia wagonjwa wengi zaidi, kuongeza ujuzi kwa wataalamu wa afya na kuwezesha hata wananchi wasio na uwezo mkubwa wa kifedha kupata huduma za matibabu zenye ubora wa hali ya juu.

Kutoka Burundi, Dkt. Nzitunga Aimee Jean Carmen Octavie wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Gitega ameishukuru Serikali ya Tanzania pamoja na uongozi wa BMH kwa kuwakaribisha na kuwapatia watoto wao matibabu salama.

Amesema mafanikio hayo yanaimarisha zaidi uhusiano wa kihistoria uliopo kati ya Tanzania na Burundi, huku yakitoa matumaini mapya kwa wagonjwa wanaohitaji huduma za kibingwa katika ukanda huo.

Naye mzazi wa mmoja wa watoto waliopatiwa upasuaji, Shedrack Nzigiyimana, amesema ameridhishwa na huduma alizopata mtoto wake na kushukuru wataalamu wa afya pamoja na Serikali ya Tanzania kwa kuwapa fursa ya kupata matibabu yaliyobadili maisha ya mtoto wake.

Amesema ukarimu na ushirikiano kati ya Tanzania na Burundi umewezesha watoto wao kupata huduma muhimu ambazo zingekuwa vigumu kuzipata kwa wakati, huku akieleza matumaini kuwa ushirikiano huo utaendelea kuwasaidia wagonjwa wengi zaidi kutoka nchi zote mbili.











Na Pamela Mollel,Arusha.

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji (Mb), amemtaka Kamishna mpya wa Uhifadhi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Massana Gibril Mwishawa, kuimarisha utendaji wa shirika hilo kwa kuhakikisha sekta ya uhifadhi na utalii inaendelea kutoa mchango mkubwa katika maendeleo ya taifa

Akizungumza jijini Arusha wakati wa hafla ya kumuapisha Kamishna huyo, Waziri Kijaji amesema uongozi mpya unapaswa kuelekeza nguvu katika kuboresha miundombinu ya hifadhi, kuongeza fursa za uwekezaji, kuanzisha bidhaa mpya za utalii na kusimamia mapato kwa ufanisi ili kuongeza mchango wa sekta hiyo kwenye uchumi wa nchi

Pia alisisitiza umuhimu wa kujenga mahusiano mazuri na wananchi wanaozunguka maeneo ya hifadhi, akieleza kuwa ushirikiano wao ni nguzo muhimu katika kulinda rasilimali za taifa

Aidha, alimwelekeza Kamishna kuhakikisha nidhamu, uadilifu, weledi na ustawi wa watumishi wa TANAPA vinaendelea kupewa kipaumbele

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya TANAPA, Mkuu wa Majeshi Mstaafu Jenerali George Waitara, amesema bodi itaendelea kushirikiana na menejimenti ya shirika hilo kwa kutoa ushauri na miongozo itakayosaidia kufanikisha malengo ya uhifadhi na maendeleo ya utalii nchini.

Aliongeza kuwa uwazi katika uendeshaji wa shughuli za shirika pamoja na utoaji wa mrejesho kwa watumishi wa ngazi mbalimbali ni muhimu katika kuongeza ufanisi na kufikia malengo yaliyowekwa

Naye Kamishna wa Uhifadhi, Massana Gibril Mwishawa, amesema ataiongoza TANAPA kwa kuzingatia misingi ya uwajibikaji, uzalendo, uadilifu na weledi, huku akisisitiza kuwa hifadhi za taifa zina nafasi muhimu katika kulinda bioanuwai, kuchochea uchumi na kusaidia utekelezaji wa miradi ya maendeleo kupitia mapato yatokanayo na utalii.

Aliongeza kuwa anamshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kumteua kushika nafasi hiyo, akiahidi kushirikiana kwa karibu na watumishi wote wa TANAPA ili kuendelea kuimarisha mafanikio ya taasisi hiyo.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi wa taasisi mbalimbali za uhifadhi, akiwemo NCAA, TFS na TAWA, pamoja na viongozi wa Serikali, wadau wa sekta ya uhifadhi na utalii, viongozi wa dini, maafisa na askari wa TANAPA.







Na Seif Mangwangi, Michuzi TV Arusha

SERIKALI imesema Mwitikio wa vijana kutaka kukopeshwa fedha kwaaji li ya kuanzisha biashara umekuwa mkubwa na wa kutia moyo baada ya baadhi ya masharti magumu yaliyokuwa yakiwashinda vijana kuondolewa.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa programu ya Kitaifa ya utoaji wa mikopo kupitia programu ya billioi 200 chini ya mfuko wa maendeleo ya vijana leo 9 Julai 2026,Jijini Arusha, Waziri wa nchi ofisi ya Rais Vijana, Joel Nananuka amesema miongoni mwa changamoto zilizokuwa zikilalamikiwa ni riba kubwa kwa wakopaji.

“Riba ilikuwa ni changamoto, na Sasa riba imeondolewa mtu akishapata mikopo na kulipa bima basi atapata mikopo wake, pia kulikuwa na changamoto ya mikopo kurejesha mapema, tunataka mtu akipata fedha aanze kufanyia kazi ndipo aanze kurejesha, mwongozo mpya ni kwamba watakaa na mkopo kwa miezi mitatu kabla ya kuanza kurejesha,” amesema.

Amesema changamoto nyingine iliyofanyiwa mabadiliko ni mtu mmoja mmoja kupata fedha kama alivyoomba badala ya kuwa katika kikundi ndio update fedha hizo kama ilivyokuwa hapo awali.

“ Ilikuwa fedha zinatolewa kwa vikundu pekee na sio mtu mmoja mmoja lakini sasa hivi kama tulivyoagizwa na Mheshimiwa Rais Samia tuondoe vikwazo vyote, basi awamu hii vijana wengi watapata mkopo Kwa namna alivyoomba bila kupitia kikundi,” amesema.

Amesema baada ya kutatuliwa Kwa changamoto hizo, jumla ya maombi 30,384 yalipokelewa kutoka maeneo mbalimbali nchini yakihusisha sekta za kilimo, mifugo, uvuvi, viwanda vidogo, biashara, ubunifu, teknolojia na huduma mbalimbali.

“ Takwimu hizi zinaonesha wazi kuwa vijana wa Tanzania si wavivu kama ambavyo wakati mwingine imekuwa ikidaiwa;

badala yake, wanahitaji mazingira yanayowapa fursa ya kuonesha uwezo wao,” amesema Nanauka na kuongeza:

“Baada ya mchakato wa kina wa tathmini uliozingatia vigezo vilivyowekwa, kwa awamu ya kwanza tunaenda kuwezesha miradi ya vijana yenye thamani ya Shilingi Bilioni 8 kupitia Mfuko wa Maendeleo ya vijana unapojaribiwa na Ofisi ya Rais - Maendeleo ya vijana,” amesema.

Amesema katika uzinduzi wa programu hiyo, katika Mkoa wa Arusha mikopo ya shilingi milioni 730 itatolewa ambapo milioni 500 zitaenda katika utafiti na utengenezaji wa dawa za binadamu, Milioni 130 zitaenda katika kiwanda cha vijana kinachotengeneza chaki zisizotoa vumbi na milioni 100 zitaenda kwa viundi vya Mama na Baba Lishe.

“ Hii ni hatua ya mwanzo ambayo itaendelea kupanuliwa kadri fedha zitakavyopatikana na tathmini za utekelezaji zitakavyoendelea kuonesha mafanikio,” amesema.

Amesema fedha hizo ni za uwekezaji wa Taifa kwa vijana wake na kwamba Serikali imewaamini na imeamua kuwekeza kwa vijana kwa matarajio kwamba watazitumia kuongeza uzalishaji, kupanua biashara, kuanzisha viwanda vidogo, kuongeza thamani ya bidhaa na kuzalisha ajira kwa vijana wengine.

“Napenda kuwasisitiza kuwa mafanikio ya programu hii hayatapimwa kwa kiwango cha fedha kilichotolewa, bali kwa matokeo yatakayopatikana. Tunataka kuona biashara zenye tija, ongezeko la mapato ya kaya, ajira mpya, ukuaji wa kampuni za vijana na mchango mkubwa wa sekta ya vijana katika pato la Taifa, “ amesema na kuongeza:

“Hivyo basi, nawasihi mtumie fedha hizi kwa malengo yaliyokusudiwa; wekeni mifumo mizuri ya usimamizi wa fedha; tunzeni kumbukumbu za biashara zenu; zingatieni misingi ya utawala bora wa biashara; na hakikisheni mnarejesha mikopo kwa wakati. Nidhamu ya fedha ndiyo msingi wa mafanikio ya biashara yoyote duniani.” Amesema.

Awali Mkuu wa Mkoa wa Arusha CPA Amos Makala amesema vijana wa Arusha wanajitambua na hawachezi na fursa na kwamba Kwa juhudi wanazoendelea nazo ana uhakika kesho yao itakuwa njema.

Mwakilishi wa benki ya CRDB, Meneja wa Benki hiyo tawi la Meru Arusha, Haika Mawalla amesema CRDB Bank inajivunia kuaminiwa na Serikali kupewa jukumu la kusimamia utekelezaji wa mpango huo wa uwezeshaji wa vijana nchini kote.

“ Hili ni jukumu kubwa na tunalipokea kwa uzito, uadilifu na uwajibikaji. Tumejipanga kuhakikisha huduma hii inawafikia vijana wengi iwezekanavyo kwa uwazi, ufanisi na weledi,” amesema.

Amesema mbali na kutoa mikopo, CRDB itaendelea kuwajengea vijana uwezo kupitia elimu ya fedha, usimamizi wa biashara na matumizi sahihi ya mikopo na kwamba wanaamini kuwa mchanganyiko wa mtaji, maarifa na nidhamu ya fedha ndio msingi wa mafanikio ya biashara na ujasiriamali endelevu.

“Tunawasihi vijana wote kuitumia fursa hii kwa ubunifu, uwajibikaji na uaminifu. Mikopo hii ni chachu ya maendeleo; itumike kuanzisha na kukuza miradi yenye tija, kuongeza ajira na kuinua uchumi wa familia na Taifa kwa ujumla,” amesema.






Na Janeth Raphael MichuziTv

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema Watanzania wanahitaji amani, usalama na utulivu badala ya vurugu na mivutano ya kisiasa, akisisitiza kuwa mazingira hayo ndiyo msingi wa Serikali kuendelea kutoa huduma bora za kijamii, kukuza uchumi na kuongeza fursa za ajira kwa wananchi.

Rais Samia ametoa kauli hiyo leo Alhamisi, Julai 9, 2026, visiwani Zanzibar wakati wa hafla ya kushuhudia utiaji saini wa Tamko la Pamoja la Maridhiano ya Kisiasa kati ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na ACT Wazalendo.

Amesema maridhiano ya kisiasa hayapaswi kutafsiriwa kama ishara ya udhaifu, bali ni alama ya ukomavu wa kisiasa unaojenga msingi wa umoja, kuheshimiana na ushirikiano miongoni mwa viongozi wenye mitazamo tofauti kwa maslahi ya taifa na wananchi.

Kwa mujibu wa Rais Samia, hatua hiyo inafungua ukurasa mpya wa kuimarisha mshikamano, amani na utulivu nchini, hususan Zanzibar, huku akihimiza siasa kujengwa katika misingi ya hoja, heshima na ustaarabu badala ya chuki, migawanyiko na mivutano isiyo na tija.

Amesema migogoro na siasa za chuki huzuia maendeleo, lakini maridhiano na siasa za staha huweka mazingira bora ya utekelezaji wa mipango ya maendeleo na kuboresha ustawi wa wananchi.

Rais Samia pia amezitaka pande zote zinazohusika na maridhiano hayo kuheshimu makubaliano yaliyofikiwa, kuendelea na mazungumzo kwa uwazi na kujenga imani ili kulinda umoja, amani na usalama wa taifa.

Akihitimisha hotuba yake, Rais Samia amesisitiza umuhimu wa kudumisha mshikamano uliojengwa kupitia maridhiano hayo.

"Hekima tuliyoionesha leo ikalindwe kwa matendo mema ya kesho, na imani tuliyoijenga kwa muda mrefu isiangushwe kwa maneno au mienendo isiyo na tija," amesema Rais Samia.

















Top News