Muungano wa watoa huduma za mawasiliano nchini (Telco Operators Consortium) umekamilisha rasmi ujenzi wa minara ya mawasiliano 758 na kukabidhi zaidi ya kilomita 1,100 za miundombinu ya nyaya za fiber optic kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hatua ambayo ni mafanikio makubwa katika utekelezaji wa mpango wa taifa wa kupanua miundombinu ya mawasiliano.

Hafla ya makabidhiano imefanyika katika kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete jijini Dodoma na kuhudhuriwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan.

Mradi huo umejengwa kupitia ushirikiano wa muda mrefu kati ya sekta ya umma na sekta binafsi (PPP), ukiwa na lengo la kuharakisha upatikanaji wa intaneti ya kasi na kuimarisha Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano (NICTBB).

Kwa mujibu wa muungano huo, mradi huo unahusisha njia kuu za fiber optic katika korido za Dodoma–Mwanza, Morogoro–Ifakara na Moshi–Rombo, zenye urefu wa takriban kilomita 1,193.

Pia unajumuisha miundombinu ya fiber ya mijini katika miji mikubwa ikiwemo Dar es Salaam, Arusha, Mbeya, Mwanza, Tanga, Moshi, Morogoro, Dodoma, Tabora, Shinyanga, Biharamulo, Makambako na Musoma. Sehemu nyingine za mradi bado ziko katika hatua za ujenzi na zitakabidhiwa baada ya kukamilika.

Rais Samia Suluhu Hassan ameupongeza muungano huo kwa mchango wake katika kuimarisha upatikanaji wa huduma za kidijitali nchini na kuongeza ushindani wa kiuchumi kupitia miundombinu bora ya mawasiliano.

Akizungumza wakati wa halfa kwa niaba ya muungano huo, Mwenyekiti wa Muungano Bw. Pierre Canton Bacara ambaye pia ni Afisa Mtendaji Mkuu wa Yas, amesema mradi huo unaonesha umuhimu wa ushirikiano endelevu kati ya Serikali na sekta binafsi katika kufanikisha malengo ya kitaifa ya uimarishaji wa mawasiliano.

Aliongeza kuwa miundombinu hiyo itaongeza upatikanaji wa huduma mbalimbali na kuchochea ukuaji wa sekta muhimu ikiwemo huduma za kifedha, biashara mtandao (e-commerce), afya na elimu kupitia mawasiliano yaliyoimarishwa.

Kwa upande wa Kampuni ya Mawasiliano ya Yas, imekuwa na jukumu kubwa la kiutendaji ndani ya muungano huo, ikishiriki katika ujenzi na usambazaji wa mtandao katika maeneo mbalimbali nchini.

Kampuni hiyo imechangia takriban asilimia 33 ya maeneo yote yaliyokamilishwa (saiti 261) na pia imeboresha mtandao wake kote nchini kutoka 2G na kuwa 4G kama sehemu ya mpango wa kisasa wa miundombinu ya mawasiliano.

Aidha, Yas Tanzania imewekeza zaidi ya TZS trilioni 1 katika miundombinu ya mtandao na kwa sasa inaendesha mojawapo ya mitandao mikubwa zaidi ya 4G na 5G nchini, inayofikia zaidi ya asilimia 95 ya wananchi.

Kampuni hiyo imesisitiza dhamira yake ya kuendelea kupanua huduma jumuishi za mawasiliano hadi maeneo ya vijijini na maeneo ambayo bado hayajafikiwa kikamilifu.

“Kadiri Tanzania inavyoendelea kuelekea kuwa kitovu cha kidijitali cha ukanda wa Afrika Mashariki, ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi utaendelea kuwa nguzo muhimu ya kuharakisha mageuzi haya,” alisema.

 Mwenyekiti wa muungano huo.Muungano huo pia umeeleza kuwa uungwaji mkono wa kisera, ikiwemo mapitio ya gharama za intaneti, utaongeza ushindani wa Tanzania kama kitovu cha mawasiliano kikanda na kusaidia ongezeko la matumizi ya data nchini.

Makabidhiano haya ya miundombinu, yanayojumuisha minara ya mawasiliano na Mkongo wa Taifa wa fiber optic, na ni sehemu ya ajenda pana ya mageuzi ya kidijitali Tanzania, chini ya Ajenda 2050, yenye lengo la kuhakikisha upatikanaji wa mawasiliano ya bei nafuu, uhakika na imara kote nchini.-






MWILI wa marehemu bondia wa zamani wa Taifa, marehemu Lucas Msomba unatarajiwa kuzikwa Jumatatu katika makaburi ya Mkuza yaliyopo Kibaha kwa Mathias mkoani Pwani.

Pichani toka kushoto ni Filbert Bayi (bingwa wa dunia wa mita mbio za 1500), Gidamis Shahanga (bingwa wa marathon wa Jumuiya ya Madola), Emmanuel Mlundwa (bingwa wa ndondi Afrika wa uzito wa flyweight), na Lucas Msomba (bingwa wa ndondi Afrika wa uzito wa lig

Kwa mujibu wa binti wa marehemu, Monica Luca Msomba, ibada ya mazishi itaanza saa nne asubuhi nyumbani kwa familia kilichopo Kibaha kwa Mathias, Mtaa wa Jamaica, barabara ya kuelekea Kambi ya Jeshi Msangani.

Ameeleza kuwa ibada ya nyumbani itafanyika kuanzia saa nne hadi saa tano asubuhi, ambapo ndugu, jamaa na marafiki watapata fursa ya kutoa heshima zao za mwisho.

Baada ya hapo, mwili wa marehemu utapelekwa Kanisa la Katoliki Mkuza kwa ajili ya ibada ya kuaga itakayofuatiwa na maziko katika makaburi ya Mkuza.

Familia imewaomba waombolezaji kufika kwa wakati ili kushiriki kikamilifu katika ratiba ya mazishi ya mpendwa wao.

Lucas Msomba, bondia wa Taifa maarufu sana miaka ya 80 hadi 90, amefariki dunia siku ya Ijumaa Aprili 10, 2026 huko nyumbani kwake Kibaha kwa Mathias, mkoa wa Pwani.

Msomba, aliyefariki dunia akiwa na umri wa miaka 72, ni mmoja wa mabondia waliowika sana ndani na nje ya nchi, akiwa na wenzie kina Mlundwa, Habibu Kinyogoli, Nassoro Michael, Isaack Mabushi, Flavian Bitegeko na wengineo.

Licha ya kuwa bingwa wa Taifa kwa muda mrefu, Msomba amekiwakilisha taifa katika mashindano mengi ya ndondi ya uzito wa welterweight ikiwa ni pamoja na Michezo ya Olimpiki ya mwaka 1980 huko Moscow

Kabla ya hapo, alijipatia heshima kubwa kwa kushinda medali ya shaba katika uzito wa light-welterweight kwenye Michezo ya Afrika ya mwaka 1978 iliyofanyika Algiers.

Msomba anakumbukwa kama miongoni mwa mabondia waliolitangaza sana jina la Tanzania kimataifa, akionesha uwezo, nidhamu na uzalendo mkubwa.

Baada ya kustaafu akawa mshauri kwa mabondia chipukizi, lakini kwa bahati mbaya hakuendelea saakapatwa na maradhi ikabidi akatwe mguu wake wa kuume.
WAZIRI wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo(Mb), amekutana na kuzungumza na Waziri wa Mambo ya Nje na Diaspora wa Jamhuri ya Seychelles Mhe. Barry Faure pembezoni mwa Mkutano wa Tisa Bahari ya Hindi jijini Port Louis, Mauritius Aprili 11,2026.

Kikao hicho, kililenga kuangalia njia za kuendelea kuimarisha uhusiano uliopo kati ya Tanzania na Seychelles ambapo viongozi hao pia walijadili masuala mbalimbali ya maslahi ya pamoja ikiwemo ushirikiano wa kisiasa, kiuchumi, na amani ya kikanda.

Tanzania na Seychelles zinashirikiana katika maeneo ya biashara na uwekezaji. Bidhaa kuu zinazouzwa Nje ni pamoja na misumari, pini ndogo (tacks), pini za kuchomelea misumari ya bati vikolezo na bidhaa zinazofanana, bidhaa za chuma au chuma kigumu, nati nazi na korosho ambapo bidhaa kuu zinazoagizwa ni nguo, samaki wa jamii ya jodari, na jodari aina ya skipjack.

Kuhusu uwekezaji katika kipindi cha kuanzia 2014 hadi 2024 Tanzania na Seychelles zimekuwa zikishirikiana katika ujenzi wa majengo ya biashara na viwanda na hivyo kusababisha ajira nchini. Tanzania na Seychelles pia zimekuwa zikishirikiana katika eneo la ulinzi na usalama pamoja na masuala ya magereza.


Mawaziri hao walielezea dhamira ya kutumia matokeo ya kikao chao kuendelea kuimarisha ushirikiano katika maeneo ya biashara, utalii na usalama, kwa lengo la kukuza maendeleo na kudumisha amani, utulivu na usalama katika ukanda wa Bahari ya Hindi.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo akisalimiana na Waziri wa Mambo ya Nje na Diaspora wa Jamhuri ya Seychelles Mhe. Barry Faure walipokutana jijini Port Louis Mauritius Aprili 11,2026 pembezoni mwa Mkutano wa Tisa Bahari ya Hindi.

Mkurugenzi Msaidizi wa Usafirishaji wa Barabara wa Wizara ya Uchukuzi Andrew Magombana akizungumza wakati kufungua mkutano Mkuu wa Kwanza wa Chama cha Wasafirishaji wa Mizigo kwa Barabara Tanzania (TRFA) uliofanyika Hoteli ya Four Point Jijini Dar es Salaam.

Mwenyekiti wa Bodi wa TRFA Vianey Rweyendela akizungumza kuhusiana na mikakati ya TRFA  katika Mkutano Mkuu wa Kwanza wa TRFA uliofanyika Hoteli ya Four Point  jijini Dar es Salaam.
Makamu Mwenyekiti waTRFA Sophia Caroline Mansoor akifunga mkutano mkuu wa Kwanza wa TRFA  uliofanyika Hoteli ya Four Point  jijini Dar es Salaam.
Afisa Mtendaji Mkuu wa TRFA Hussein Wandwi akitoa taarifa kwa Wanachama  katika Mkutano Mkuu wa Kwanza wa TRFA uliofanyika Hoteli ya Four Point  jijini Dar es Salaam.

Na Mwandishi Wetu
SERIKALI kupitia Wizara ya Uchukuzi imesema imeanza kuchukua hatua za kutatua changamoto zinazokwamisha sekta ya usafirishaji nchini, ikiwemo msururu wa tozo unaowakabili wasafirishaji, foleni ya muda mrefu katika mpaka wa Tunduma na tozo za matumizi ya barabara zinazotozwa kwa madereva wa Tanzania nchini Zambia.

Hayo yamebainishwa katika Mkutano Mkuu wa Kwanza wa Chama cha Wasafirishaji wa Mizigo kwa Barabara Tanzania (TRFA) uliofanyika jijini Dar es Salaam, ambapo wadau wa sekta hiyo waliwasilisha changamoto mbalimbali zinazoathiri uendeshaji wa biashara.

Akizungumza katika mkutano huo, Afisa Mtendadaji Mkuu wa TRFA Hussein Wandwi alisema kuwa moja ya changamoto kubwa ni tozo za barabara nchini Zambia ambazo zimeongeza gharama za uendeshaji kwa wasafirishaji wa Tanzania.

“Moja ya changamoto kubwa ni tozo mpya za barabara za Zambia. Kama wenzetu wanatoza malori yetu, nasi tunapaswa kuwatoza malori yao,” alisema Wandwi.

Alisema pia kuwa wasafirishaji wanakabiliwa na changamoto ya tozo kutoka Halmashauri na Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri Ardhini (LATRA), ikiwemo kodi ya huduma iliyopunguzwa kutoka asilimia 0.3 hadi 0.25 ya mauzo ya kila robo mwaka, ambayo bado inalalamikiwa na wadau.

Aidha, Wandwi aliitaka Serikali kuangalia upya mfumo wa mawakala wa usafirishaji wasio rasmi ili waweze kusajiliwa rasmi na kutambuliwa, sambamba na kusajiliwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), jambo litakalosaidia kuongeza uwazi na ukusanyaji wa mapato.

Akizungumza wakati wa kufungua Mkutano Mkuu wa Kwanza wa TRFA Mkurugenzi Msaidizi wa Usafiri wa Barabara kutoka Wizara ya Uchukuzi, Andrew Magombana, alisema serikali imepokea malalamiko kuhusu tozo za Zambia na tayari imeanzisha mazungumzo na Serikali ya Zambia ili kupata ufumbuzi wa kudumu.

Akizungumzia foleni katika mpaka wa Tunduma, Magombana alisema serikali za Tanzania na Zambia zinafanya kazi kwa pamoja ili kuhakikisha mpaka huo unakuwa sehemu ya kupita badala ya kuwa sehemu ya kusubiri, huku hatua za kuongeza mageti zikitarajiwa kupunguza msongamano.

Naye Makamu Mwenyekiti wa TRFA, Sophia Caroline Mansoor, alisema chama hicho kitaendelea kushirikiana na serikali ili kutatua changamoto zilizopo, akisisitiza umuhimu wa kuimarisha mazingira ya uwekezaji katika sekta ya usafirishaji kwa kuwa Tanzania ni kitovu cha usafirishaji kwa nchi nyingi kupitia bandari zake.

Mansoor alisema kuboresha mazingira ya biashara katika sekta ya usafirishaji kutachangia kwa kiasi kikubwa katika kukuza uchumi wa nchi na kuvutia uwekezaji zaidi.


Na Munir Shemweta, WANMM Nairobi

Serikali ya Tanzania imeendelea kusisitiza dhamira yake ya kuboresha makazi holela na kuyageuza kuwa maeneo rasmi, salama na yenye huduma bora, ikiwa ni sehemu ya kukabiliana na kasi kubwa ya ukuaji wa miji nchini.

Hayo yameelezwa mwishoni mwa wiki jijini Nairobi nchini Kenya na Waziri wa Ardhi. Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo katika mjadala maalum uliofanyika pembezoni mwa Kongamano la Pili la Miji Afrika (2ND Afrika Urban Forum), ambapo washiriki walipata fursa ya kujadili mbinu jumuishi za kuleta mageuzi katika makazi holela.

Amesema, Tanzania kama zilivyo nchi nyingi zinazoendelea, inashuhudia ongezeko kubwa la watu wanaohamia mijini, hali inayosababisha shinikizo katika upangaji wa miji, utoaji wa makazi, usimamizi wa ardhi pamoja na huduma za kijamii na kiuchumi.

Ameeleza kuwa, katika kipindi cha zaidi ya nusu karne, idadi ya watu wanaoishi mijini imeongezeka kwa kasi kutoka asilimia 5.7 mwaka 1967 hadi kufikia asilimia 34.9 mwaka 2022, huku makadirio yakionesha kuwa ifikapo mwaka 2050 idadi hiyo itafikia asilimia 59.

‘’Ukuaji huu unaifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zinazoongoza kwa kasi ya ukuaji wa miji katika ukanda wa Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara’’. amesema

Kwa mujibu wa Waziri huyo wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, ukuaji huo umeambatana na kuongezeka kwa makazi holela, ambapo takribani asilimia 67.3 ya makazi yote mijini yapo katika maeneo yasiyopangwa.

Kutokana na changamoto hiyo, Dkt Akwilapo ameeleza kuwa, Serikali ya Tanzania imechukua hatua za kimkakati zinazolenga kuboresha makazi hayo badala ya kuyabomoa, kwa kutumia mbinu za upangaji shirikishi, uboreshaji wa miundombinu na utoaji wa huduma muhimu kama maji, barabara na umeme.

Amesema, Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Makazi ya Watu ya mwaka 2000 pamoja na Sera ya Ardhi ya mwaka 1995 iliyoboreshwa mwaka 2023, zinaelekeza wazi kuwa makazi holela yataboreshwa na kurasimishwa ili kuhakikisha wakazi wanapata haki ya umiliki wa ardhi na huduma za msingi.

Aidha, ameweka wazi kuwa, Serikali imeendelea kutekeleza mpango wa urasimishaji wa makazi holela kwa kuwapatia wananchi hati miliki za ardhi, hatua inayochochea uwekezaji na kuwezesha wananchi kupata mikopo kutoka taasisi za kifedha.

‘’Mpango huo pia unalenga kubadilisha rasilimali zisizo rasmi kuwa mali zenye tija katika uchumi wa nchi’. amesema

Aidha, Dkt Akwilapo amesema, Serikali ya Tanzania pia imeanzisha programu maalum ya upangaji upya wa ardhi (land readjustment) inayolenga kuboresha maeneo chakavu yaliyopo katikati ya miji, ili kuyafanya yaweze kutumika kwa ufanisi zaidi kiuchumi na kijamii.

Akihitimisha wasilisho lake Waziri huyo wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi alisisitiza kuwa makazi holela hayapaswi kuonekana kama tatizo pekee, bali kama sehemu ya fursa za kiuchumi na ubunifu kwa wananchi wengi.

Aalitoa wito kwa nchi za Afrika kushirikiana katika kuunganisha mipango rasmi ya miji na hali halisi ya makazi holela, ili kujenga miji himilivu, jumuishi na inayokidhi mahitaji ya wote bila kumuacha mtu nyuma, kwa kuzingatia malengo ya Ajenda ya Maendeleo Endelevu ya mwaka 2030.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akiwasilisha taarifa ya hali ya urasimishaji makazi holela wakati wa mjadala maalum uliofanyika pembezoni mwa Kongamano la Pili la Miji Afrika (2ND Afrika Urban Forum), ambapo washiriki walipata fursa ya kujadili mbinu jumuishi za kuleta mageuzi katika makazi holela. 
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akiwa na mawaziri wenzake kutoka Ghana Mhe. Kenneth Gilbert Adjei, Waziri wa Ujenzi, Nyumba na Rasilimali za Maji (kushoto) na Malawi Mhe. Chimwemwe Chipungu, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Miji (wa pili kulia) wakifuatilia uwasilishwaji taarifa ya hali ya makazi holela kutoka kwa Mhe. Balla Moussa Fofana, Waziri wa Mipango Miji, Serikali za Mitaa na Maendeleo ya Maeneo Senegal wakati wa mjadala maalum uliofanyika pembezoni mwa Kongamano la Pili la Miji Afrika (2ND Afrika Urban Forum) jijini Nairobi nchini Kenya mwishoni mwa wiki.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (wa pili kushoto) Mhe. Kenneth Gilbert Adjei, Waziri wa Ujenzi, Nyumba na Rasilimali za Maji kutoka Ghana (kushoto) na Mhe. Chimwemwe Chipungu, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Miji Malawi (wa pili kulia) wakifuatilia uwasilishwaji taarifa ya hali ya makazi holela wakati wa mjadala maalum uliofanyika pembezoni mwa Kongamano la Pili la Miji Afrika (2ND Afrika Urban Forum) jijini Nairobi nchini Kenya mwishoni mwa wiki.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akiwa na mawaziri wenzake kutoka nchi za Ghana, Malawi na Senegali wakati wa mjadala maalum uliofanyika pembezoni mwa Kongamano la Pili la Miji Afrika (2ND Afrika Urban Forum), ambapo washiriki walipata fursa ya kujadili mbinu jumuishi za kuleta mageuzi katika makazi holela. 
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akichangia hoja wakati wa mijadala iliyofanyika pembezoni mwa Kongamano la Pili la Miji Afrika (2ND Afrika Urban Forum) jijini Nairobi nchini Kenya mwishoni mwa wiki.
Sehemu ya washiriki wa mijadala mbalimbali iliyofanyika pembezoni mwa Kongamano la Pili la Miji Afrika (2ND Afrika Urban Forum) jijini Nairobi nchini Kenya mwishoni mwa wiki. (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)





Uharibifu wa Ziwa Victoria: Matokeo ya Shughuli za Kibinadamu Yaanza Kuonekana Wazi

Katika miaka ya karibuni, kumekuwa na ongezeko kubwa la shughuli za kibinadamu kandokando ya Ziwa Victoria, hali ambayo sasa imeanza kuleta athari zinazoonekana wazi katika mfumo wa ikolojia wa ziwa hilo.
Uchunguzi uliofanywa na Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO), ukiongozwa na Katibu Mkuu wake, Boniventura Mwalongo, umebaini changamoto kadhaa zinazolikumba ziwa hilo. Ziara hiyo ilifanyika katika eneo la Kigoto, Mwanza, kwa kushirikiana na Taasisi ya Haki za Binadamu (TAHURI).

Miongoni mwa changamoto zilizobainika ni pamoja na uwepo wa magugu vamizi, matumizi holela ya rasilimali za ziwa, pamoja na uchafuzi wa maji unaotokana na majitaka yasiyodhibitiwa.

Aidha, kupungua kwa kina cha maji kumetajwa kuwa matokeo ya moja kwa moja ya uharibifu wa maeneo ya kinga ya fukwe, jambo linalochangia kuongezeka kwa tope na mchanga ndani ya ziwa. Hali hii inaathiri kwa kiasi kikubwa mazalia ya samaki na kusababisha kupungua kwa uzalishaji wa rasilimali hiyo muhimu.

Wataalamu wanaonya kuwa endapo hali hii itaendelea, usalama wa chakula, ajira za wavuvi na uchumi wa maeneo yanayozunguka ziwa hilo vitakuwa hatarini.


Mbunge wa Jimbo la Namtumbo Dk Juma zuberi Homera Aprili 11, 2026, Amekabidhi rasmi magari mawili kwa Ofisi ya TANESCO wilayani Namtumbo, hatua inayolenga kuongeza ufanisi na kasi ya utoaji wa huduma ya umeme katika jimbo letu.

Kupatikana kwa magari haya ni sehemu ya juhudi endelevu za kuboresha miundombinu na kuimarisha upatikanaji wa huduma muhimu kwa wananchi, hususan katika maeneo ya vijijini na pembezoni.

Magari hayo yanatarajiwa kurahisisha shughuli za kiutendaji, ikiwemo usimamizi wa miradi ya umeme, matengenezo ya miundombinu, pamoja na kushughulikia changamoto za huduma kwa wakati.

Aidha Mh Mbunge Amepongeza TANESCO kwa jitihada zake madhubuti katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya umeme kwa uhakika, hatua ambayo inaendelea kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika maeneo mbalimbali.

"Ninawapongeza watumishi wa taasisi hiyo kwa kujituma kwao na kuwasihi kuyatunza vyema magari hayo ili yaweze kudumu na kutoa tija iliyokusudiwa. Matumizi sahihi ya rasilimali hizi ni muhimu katika kufanikisha azma ya kuwahudumia wananchi kwa ufanisi zaidi".









Timu ya mpira wa miguu ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki (NJE Sports) imepoteza kwa mabao 3–2 dhidi ya timu ya Ubalozi wa Umoja wa Ulaya katika mechi ya kirafiki iliyochezwa Aprili 11, 2026, kwenye Uwanja wa John Merlin, jijini Dodoma.

Akizungumza mara baada ya mchezo huo, Mgeni Rasmi ambaye ni Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mheshimiwa James Milya (Mb), amezipongeza timu zote mbili kwa kuonesha ushindani wa kirafiki na kudumisha mshikamano. Amesema michezo ya aina hiyo ina mchango mkubwa katika kuimarisha ushirikiano, urafiki na diplomasia kati ya taasisi na mataifa.

Ameongeza kuwa mechi hiyo ni sehemu ya juhudi za kukuza diplomasia ya michezo, sambamba na kuendeleza uhusiano mzuri uliopo kati ya Wizara na Ubalozi wa Umoja wa Ulaya.

Mchezo huo pia ulihudhuriwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Said Shaib Mussa, ambaye amesema kuwa pamoja na ushindani uliokuwepo uwanjani, lengo kuu la mchezo huo lilikuwa kuimarisha uhusiano kati ya pande husika, akisisitiza kuwa huo ndio ushindi mkubwa zaidi kuliko mabao.

Kwa upande wake, kiongozi wa timu ya Ubalozi wa Umoja wa Ulaya, Bw. Ally Mwinchade, amesema ameridhishwa na kiwango cha ushindani kilichooneshwa na timu zote mbili, akieleza kuwa mchezo huo umeimarisha zaidi uhusiano wa kirafiki kati ya pande hizo.

Ameongeza kuwa ushindi huo si matokeo ya uwanjani pekee, bali pia ni ishara ya mshikamano, ushirikiano na dhamira ya kuendeleza diplomasia kupitia michezo. Aidha, ameipongeza timu ya NJE Sports kwa kuonesha mchezo mzuri na kuahidi kuendeleza ushirikiano huo katika michezo ijayo.















Na Munir Shemweta, WANMM Nairobi

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt Leonard Akwilapo, amekutana na kufanya mazungumzo na Afisa Mtendaji Mkuu wa Shelter Afrique Bw. Thierno-Habib Hann jijini Nairobi, nchini Kenya.

Viongozi hao wawili wamekutana pembezoni mwa Kongamano la Miji Afrika (2nd Africa Urban Forum) lililofanyika kuanzia Aprili 8 hadi 10, 2026 nchini Kenya, na kukutanisha mataifa mbalimbali Barani Afrika kwa lengo la kubadilishana uzoefu na suluhisho bunifu katika kukabiliana na changamoto za maendeleo ya miji na makazi.

Dkt Akwilapo na Bw.Thierno-Habib Hann katika kikao chao walijadili masuala mbambali yanayohusu uimarishaji wa upatikanaji wa makazi nafuu kwa wananchi pamoja na ushirikiano kati ya serikali na taasisi za kifedha katika kufanikisha azma hiyo.

Shelter Afrique ni taasisi ya kifedha ya kimataifa inayolenga kusaidia maendeleo ya makazi Barani Afrika, huku makao makuu yake makuu yakiwa jijini Nairobi nchini Kenya.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (Kulia) akizungumza na Mtendaji Mkuu wa Shelter Afrique Bw.Thierno-Habib Hann jijini Nairobi, Kenya walipokutana pembezoni mwa Kongamano la pili la Miji Afrika (2ND Africa Urban Forum) lilofanyika nchini humo.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (Kushoto) na Mtendaji Mkuu wa Shelter Afrique Bw.Thierno-Habib Hann wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kikao chao jijini Nairobi, Kenya, walipokutana pembezoni mwa Kongamano la pili la Miji Afrika lilofanyika nchini humo.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (Kulia) akitambulishwa baadhi ya maafisa wa taasisi ya Shelter Afrique alipokutana na Mtendaji Mkuu wa taasisi hiyo Bw.Thierno-Habib Hann pembezoni mwa Kongamano la pili la Miji Afrika (2nd Africa Urban Forum) lilofanyika jijini Nairobi nchini Kenya. (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)

 




Top News