Naibu Waziri wa Uchukuzi David Kihenzile, ameshiriki Mkutano wa Kimataifa wa masuala ya Uchukuzi (NCT), mkutano uliofanyika katika Ukumbi wa Gallagher Estate, uliopo Johannesburg, Afrika Kusini. Mkutano huo ulifunguliwa na Rais wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa.

Sambamba na ushiriki huo, Naibu Waziri pia ameshiriki katika Mjadala wa Mawaziri wa Uchukuzi ukiwa na Mada isemayo: “Leadership and Governance in the Implementation of an Integrated, Sustainable and Safe Transport System that Promotes Inclusive Economic Growth, Job Retention and Social Development in Southern Africa.”

Wakati wa Mjadala huo, Naibu Waziri ameeleza hatua mbalimbali zilizofikiwa na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuendeleza miundombinu, ikiwemo Uwekezaji mkubwa katika Reli ya Kisasa (SGR); maboresho ya Bandari; Viwanja vya Ndege na miundombinu ya Barabara.

Aidha, ameeleza kuwa Serikali ya Tanzania inaendelea kuweka mazingira rafiki ya Uwekezaji na kuwakaribisha Wawekezaji kushiriki katika miradi mbalimbali ya maendeleo ya Sekta ya Uchukuzi, kwa lengo la kuimarisha biashara; kuongeza ushindani wa kiuchumi na kukuza maendeleo ya kikanda.













Na; Mwandishi Wetu, Unguja
TIMUya Kwahani FC imetwaa ubingwa wa Masauni Cup baada ya kuichapa Mwembeladu FC kwa changamoto ya mikwaju ya penati 1-0 baada ya sare ya bao 1-1 katika muda wa kawaida na kujinyakulia kombe pamoja na kitita cha shilingi milioni tano.

Kwahani FC ndio walitangulia kupata bao katika muda wa kawaida lililofungwa na Abdalla Himidi kabla ya Mwembeladu FC kusawazisha dakika za jioni likifungwa na Tariq Mzee na kuzifanya timu hzio kwenda kwenye mikwaju ya penati.

Penalti ya Mundhir Omar Hassan ndio iliyoipa ubingwa Kwahani FC ambayo ilitinga fainali kwa kuichapa Kwalinatu FC bao 2-1 katika mchezo wa nusu fainali wakati Mwembeladu FC iliyojinyakulia kombe na shilingi 2,000,000 ilipenya kwa penati 3-1 dhidi ya Kiswandui.

Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo Zanzibar Mhe. Riziki Pembe Juma amesema wizara itaendelea kushirikiana na wadau wa soka nchini ili kuhakikisha malengo ya Serikali ya kuibua na kuendeleza vipaji vya vijana kupitia mchezo huo yanafikiwa, sambamba na kuwapatia fursa za ajira ndani na nje ya Zanzibar.

Mhe. Riziki amesema Serikali ya Zanzibar chini ya uongozi wa Rais Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi ina dhamira ya dhati ya kuona mpira wa miguu unakuwa chombo cha kuwainua vijana kiuchumi pamoja na kuwawezesha kujenga mustakabali wao.

Alisema lengo la Rais ni kuhakikisha vijana wa Zanzibar wanatumia vipaji vyao vya soka kupata ajira na kujitambulisha kimataifa, kama ambavyo baadhi ya wachezaji wameanza kufanya, akitolea mfano wa mchezaji Feisal Salum ambaye amekuwa kielelezo cha mafanikio kwa vijana wanaocheza mpira wa miguu.

“Tunataka kuona vijana wengi zaidi kama kina Feisal Salum wanaibuka na kupeperusha bendera ya Zanzibar ndani na nje ya nchi kupitia mchezo wa mpira wa miguu,” alisema Waziri huyo.

Alieleza kuwa kutokana na dhamira hiyo, Serikali inaendelea kuwekeza katika ujenzi na uimarishaji wa miundombinu ya michezo katika wilaya na mikoa mbalimbali ili kutoa fursa kwa vijana wengi kushiriki michezo na kuendeleza vipaji vyao.

Aidha, alisema mashindano ya soka yanayoandaliwa katika majimbo yana mchango mkubwa katika kuibua vipaji vipya na kuwapa vijana sehemu sahihi ya kutumia muda wao kwa shughuli zenye manufaa badala ya kujihusisha na mambo yasiyofaa.

“Uwepo wa mashindano haya ni jambo zuri kwa sababu yanawawezesha vijana kukutana, kushindana na pia kuimarisha vipaji vyao, hata wazo la kuwa na timu za taifa za majimbo ni zuri kwani litasaidia kuongeza ushindani na kuimarisha maendeleo ya soka,” alisema.

Aliongeza kuwa mashindano hayo pia yanasaidia kujenga mshikamano na uelewano miongoni mwa vijana kutoka maeneo mbalimbali, jambo ambalo ni muhimu katika kuimarisha umoja na maendeleo ya jamii.

Kutokana na hilo, alimpongeza Mbunge wa Jimbo hilo kwa juhudi zake za kuanzisha mashindano hayo akisema hatua hiyo imewasaidia vijana wengi kujikita katika michezo na kujiepusha na vitendo visivyofaa katika jamii.

Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Kikwajuni Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni, alisema mashindano hayo yameanzishwa kwa lengo la kuwapa vijana fursa ya kuonesha vipaji vyao pamoja na kuwaunganisha vijana wa jimbo hilo kupitia michezo.

Mbali na hilo, alisema michezo ni nyenzo muhimu katika kujenga umoja, mshikamano na nidhamu miongoni mwa vijana, hivyo ni vyema kwa jamii kuendelea kuunga mkono juhudi za kuendeleza sekta ya michezo katika ngazi za chini.

Alieleza kuwa kupitia mashindano hayo vijana wengi wamepata nafasi ya kuonekana na kuonesha uwezo wao, jambo ambalo linaweza kuwasaidia kufikia malengo yao ya kuwa wachezaji bora na hata kupata fursa ya kucheza katika timu mbalimbali za ndani na nje ya Zanzibar.

Aidha, aliwataka vijana wanaoshiriki mashindano hayo kuzingatia nidhamu, kuheshimu sheria za mchezo na kudumisha mshikamano ili mashindano hayo yaweze kufikia malengo yaliyokusudiwa.


Na Mwandishi Wetu, London
WAZIRI wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa, ametangaza kuwa Tanzania iko tayari kushirikiana na wawekezaji wa kimataifa katika kukuza Sekta ya Afya na Sayansi , akisisitiza kuwa taifa linaelekea kuwa kitovu cha uzalishaji wa dawa na bidhaa za afya barani Afrika.

Akizungumza leo jijini London kwa niaba ya Waziri Mchengerwa kwenye Jukwaa la Uwekezaji la Afya na Sayansi ikiwa ni jitihada za Serikali za kuleta mageuzi makubwa katika uwekezaji wa viwanda vya ndani vya uzalishaji wa bidhaa za afya na vifaa tiba Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia eneo la Dawa na vifaaa tiba Emmanuel Tayari amewahakikishia wawekezaji dhamira ya dhati ya Serikali ya kuweka mazingira rafiki na wezeshi kwa wawekezaji kufanya uwekezaji wa viwanda vya dawa na vifaa Tiba nchini Tanzania.

Jukwaa hiyo limeratibiwa na Ubalozi wa Tanzania nchini Uingereza na Wizara ya Afya ambapo Mhe. Balozi Mbelwa Kairuki na upande wa Wizara Dkt. Seif A. Shekalaghe, Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Emmanuel Tayari Naibu Katibu Mkuu anayesimamia Dawa na Vifaa Tiba, Dkt. Grace Magembe Mganga Mkuu wa Serikali wamehudhuria. Aidha, wwngine ni Watendaji kutoka TISEZA, TMDA, MSD, MUHAS pamoja na wataalam wa Kikosi Kazi cha Kuharakisha Uwekezaji wa Dawa (PIAT) nchini.

Alibainisha kuwa juhudi hizo zinaungwa mkono kikamilifu na Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ambaye anaipa kipaumbele ajenda ya uwekezaji katika afya kama sehemu ya kuimarisha usalama wa afya, maendeleo ya viwanda na ushirikiano wa kimkakati.

Katika hotuba yake, Mchengerwa alieleza kuwa Tanzania sasa inaiona sekta ya afya si tu kama huduma ya kijamii, bali pia kama injini ya ukuaji wa uchumi. “Tunataka kuwa zaidi ya soko la bidhaa za afya zinazoagizwa kutoka nje. Tunataka kuwa kitovu cha uzalishaji, ubunifu na usambazaji wa kikanda,” alisema.

Alisisitiza kuwa uzoefu wa janga la UVIKO-19 umeonesha umuhimu wa nchi kuwa na uwezo wa ndani wa kuzalisha dawa, chanjo na vifaa tiba, akionya kuwa utegemezi mkubwa wa uagizaji kutoka nje unaweza kuhatarisha upatikanaji wa huduma muhimu wakati wa dharura.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, Tanzania imeweka mazingira rafiki kwa uwekezaji, ikiwa ni pamoja na uthabiti wa uchumi, idadi kubwa ya watu zaidi ya milioni 65, na mageuzi ya mfumo wa bima ya afya yatakayosaidia kuongeza mahitaji ya huduma za afya kwa utaratibu unaotabirika.

Aliongeza kuwa nafasi ya Tanzania katika Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) inaipa nchi faida ya kipekee ya kuhudumia soko kubwa la kikanda, jambo linalovutia zaidi wawekezaji.

Katika hatua ya kuimarisha sekta hiyo, serikali inaendelea kuendeleza Eneo Maalum la Kiuchumi la Dawa la Mloganzila pamoja na vituo vya uzalishaji wa dawa katika maeneo ya Mloganzila na Kibaha. Pia imeanzisha Kikosi Kazi cha Kuharakisha Uwekezaji wa Dawa (PIAT) kwa lengo la kurahisisha taratibu na kuharakisha uwekezaji wa kimkakati.

Mchengerwa alisisitiza kuwa Tanzania haitaki kuwa soko la teknolojia zilizopitwa na wakati au bidhaa duni, bali inalenga uzalishaji wa dawa za kisasa zinazokidhi viwango vya kimataifa. “Dawa duni hugharimu maisha. Hatuwezi kuendelea kuwa soko la dawa za jana wakati dunia imeendelea,” alionya.

Alihimiza wawekezaji kuangalia fursa zilizopo katika uzalishaji wa dawa, vifaa tiba, uchunguzi wa magonjwa, mifumo ya usambazaji, pamoja na utafiti na maendeleo ya rasilimali watu.

Kwa upande wake, alisema Uingereza ina nafasi muhimu katika kushirikiana na Tanzania kutokana na uzoefu wake katika teknolojia ya afya, utafiti na uwekezaji, akikaribisha ubia wa kimkakati utakaosaidia kukuza sekta hiyo.

Akihitimisha, Waziri Mchengerwa alitoa wito kwa wawekezaji wa kimataifa kuchangamkia fursa zilizopo nchini Tanzania, akisisitiza kuwa serikali iko tayari kuwezesha mazingira bora ya uwekezaji.

“Fursa ipo, soko linakua, na dhamira ni thabiti. Tunakaribisha wawekezaji kushirikiana nasi kujenga mustakabali wa afya barani Afrika,” alisema.

Katika Jukwaa hilo pia Meneja wa Biashara na Maendeleo, Philip Conradi wa Kampuni kubwa Duniani ya uzalishaji wa Bidhaa za Afya- Sartorius alihudhuria

Na Karama Kenyunko Michuzi Tv
UZAZI wa mpango si mjadala wa kiafya pekee, bali ni ajenda ya maendeleo ya taifa. Ni nyenzo inayogusa afya ya mama na mtoto, ustawi wa familia, nguvu kazi ya vijana na mustakabali wa uchumi wa nchi. Nchini Tanzania, pamoja na jitihada za serikali na wadau wa maendeleo, bado kuna changamoto ya uelewa mdogo, dhana potofu na upatikanaji wa huduma hasa kwa vijana.


Kwa mujibu wa tafiti za afya ya uzazi (TDHS), wastani wa mwanamke wa Kitanzania huzaa zaidi ya watoto wanne katika maisha yake ya uzazi. Aidha, chini ya nusu ya wanawake walio kwenye ndoa hutumia njia za kisasa za uzazi wa mpango. Hii inaashiria pengo la uhitaji wa huduma, hali inayochochea mimba zisizotarajiwa na kuathiri mipango ya familia na taifa kwa ujumla.
Maana na umuhimu wa uzazi wa mpango


Mtaalamu mwandamizi wa masuala ya afya ya uzazi, jinsia na familia, Dkt Katanta Simwanza, anasema dhana ya uzazi wa mpango ni kupata mtoto kwa kupangilia kutokana na makubaliano ya wenza wote wawili.

Anasema kitaalamu mimba moja hadi nyingine inashauriwa ipishane kwa miaka miwili hadi mitano ili kulinda afya ya mama na mtoto.
Kwa mujibu wake, uzazi wa mpango una faida nyingi kwa familia kwani huwapa wazazi muda wa kufanya shughuli za kiuchumi, kuimarisha mahusiano, na kumpa mama nafasi ya kurejesha afya yake baada ya ujauzito.

“Uzazi wa mpango unasaidia mtoto kupata huduma bora, afya njema na kukua katika mazingira mazuri pasipo changamoto,” anasema.
Anabainisha kuwa familia ambazo hazipangi uzazi hukabiliwa na changamoto nyingi zikiwemo uchovu wa kiafya kwa wazazi, watoto kudhoofu kiafya, ukosefu wa elimu na wakati mwingine kunyanyapaliwa katika jamii.

Aidha, anasema mimba zisizo na mpangilio zinaweza kuongeza hatari ya matatizo ya kiafya kwa mama ikiwemo kutoka mimba au kuzaa mtoto mfu.
Takwimu za Wizara ya Afya zinaonyesha kuwa ujauzito wa utotoni na mimba za mfululizo huongeza uwezekano wa vifo vya mama na mtoto.

Kwa mujibu wa Dk Simwanza, matumizi ya njia za uzazi wa mpango pia yanaweza kupunguza hatari za kijamii kwa watoto.
“Kwenye jamii zetu kuna watoto wengi ambao ni matokeo ya wazazi kutofuata uzazi wa mpango, baadhi huishia kulelewa mitaani au katika familia nyingine,” anasema.

Anaongeza kuwa bila mpangilio mzuri wa uzazi, familia nyingi hukosa utulivu wa mawasiliano na ushirikiano jambo linaloweza kusababisha changamoto za kiafya, lishe duni na hata vitendo vya ukatili wa kijinsia.

Ushiriki wa wanaume bado mdogo
Licha ya uwekezaji unaofanywa na serikali na wadau katika kuboresha huduma za uzazi wa mpango, matumizi yake bado yako chini ya asilimia 35.
Dk Simwanza anasema hali hiyo inachangiwa na sababu mbalimbali ikiwemo mitazamo ya kidini, dhana potofu na ukosefu wa ushiriki wa wanaume katika maamuzi ya uzazi.

“Uwekezaji mkubwa ulilenga zaidi wanawake wakati mara nyingi wanaume ndio watoa maamuzi katika familia,” anasema.
Anaongeza kuwa wanaume wanapaswa kutambuliwa kama wenza na wateja wa huduma za uzazi wa mpango ili waweze kushiriki kikamilifu katika kupanga familia zao.
Vijana na changamoto za kupata taarifa sahihi
Ripoti za kitaifa zinaonyesha kuwa zaidi ya theluthi moja ya wasichana hupata ujauzito kabla ya kutimiza miaka 18. Mimba za utotoni huchangia utoro wa shule, ndoa za mapema na kuendeleza mzunguko wa umaskini wa kizazi hadi kizazi.
Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mwanafunzi mwa Mwaka wa pili, Rehema Hamidu anasema kikwazo kikubwa kwa vijana ni hofu na aibu wanapohitaji kupata huduma za uzazi wa mpango.

“Tunaogopa kuonekana tumekosea kimaadili hasa tukikutana na wahudumu wa afya wakubwa au tunaowafahamu,” anasema.
Anaongeza kuwa ukosefu wa faragha katika baadhi ya vituo vya afya na utegemezi wa taarifa kutoka mitandao ya kijamii huongeza mkanganyiko kwa vijana.

Kwa upande wake Mark Emmily anasema dhana potofu zimeathiri maamuzi ya vijana wengi, huku baadhi wakiamini kuwa uzazi wa mpango husababisha ugumba au saratani.
Hata hivyo, Dkt Simwanza anasisitiza kuwa hakuna ushahidi wa kisayansi unaoonyesha kuwa matumizi ya njia za uzazi wa mpango husababisha ugumba wa kudumu.
Mtazamo wa dini katika uzazi wa mpango
Katika jamii ambayo dini ina ushawishi mkubwa katika maamuzi ya familia, viongozi wa dini pia wanaona umuhimu wa kutoa elimu sahihi kuhusu afya ya uzazi.

Mchungaji na mdau wa maendeleo James Mlali anasema dini nyingi zinakubaliana kuhusu umuhimu wa kupishanisha watoto kwa muda unaofaa ili kulinda afya ya mama na mtoto.

“Dini zote zinahimiza kutoa nafasi kati ya mtoto na mtoto angalau miaka miwili, ambayo pia ni kipindi cha msingi cha unyonyeshaji wa mtoto,” anasema.

Kwa mujibu wake, mafundisho ya dini yanaweka msingi wa uwajibikaji katika malezi ya familia.

Anasema katika Biblia Takatifu kuna mafundisho yanayohimiza watu kuwajibika kwa familia zao na kuhakikisha wanawapatia watoto mahitaji muhimu.

Anaongeza kuwa hata katika Qur'an mafundisho yanasisitiza umuhimu wa kuwahudumia wake na watoto kwa haki na uwezo.

Mlali anaona taasisi za dini zina nafasi kubwa katika kuwapa vijana elimu sahihi kuhusu masuala ya familia, afya ya uzazi na maadili.

“Ni muhimu vijana wakapewa elimu sahihi wawapo misikitini na makanisani ili waweze kufanya maamuzi sahihi kuhusu maisha yao ya baadaye,” anasema.

Anasisitiza kuwa mila za kitamaduni kama jando na unyago zinaweza pia kuboreshwa ili kujumuisha elimu ya afya ya uzazi na kuwasaidia vijana kuelewa masuala ya familia kwa kina.

"Uzazi wa mpango ni kitu muhimu sana kwa vijana kwani vijana ambao hawana majukumu ya kifamilia huduma za afya ha uzazi ni nzuri katika kuamua wakati wa kuzaa, kupishanisha kwa muda gani na mara ngapi wabebe mimba hiyo muhimu kwa afya zao na kuweka mipango ya maendeleo," anasema.

Mchungaji Mlali anasema kupanga uzazi ni muhimu katika kuwapatia watoto huduma za lishe, elimu na masuala ya kisaikolojia.

Anasisitiza kwamba kuna makanisa yanaunga mkono njia za uzazi wa mpango wa asili na kisasa na Kanisa Katoliki linahimiza njia za asili pekee kulingana na mahitaji yao na afya ya wanaohitaji huduma hizo.

Hatua za serikali na wadau
Serikali imeendelea kuimarisha sera na mipango ya kuboresha huduma za uzazi wa mpango kupitia Wizara ya Afya pamoja na ushirikiano wa wadau wa maendeleo.

Hatua hizo zinahusisha kuandaa wataalamu wa kutoa huduma za uzazi wa mpango wa muda mfupi na mrefu, pamoja na kusambaza elimu katika maeneo ya vijijini kupitia huduma za mkoba.

Aidha, katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 uzazi wa mpango umepewa kipaumbele kama sehemu ya kupunguza vifo vya mama na mtoto, mimba zisizotarajiwa na vitendo vya ukatili wa kijinsia.

Kwa ujumla, uzazi wa mpango ni zaidi ya suala la afya ni mkakati wa kijamii na kiuchumi unaogusa maendeleo ya taifa. Ushirikiano kati ya serikali, wataalamu wa afya, viongozi wa dini na jamii kwa ujumla unaweza kusaidia kuvunja dhana potofu na kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa kupanga uzazi.

Kuwapa vijana taarifa sahihi, huduma rafiki na mazingira salama ya kuuliza maswali ni hatua muhimu katika kulinda mustakabali wa taifa. Tanzania yenye vijana wenye taarifa sahihi na maamuzi bora ndiyo Tanzania yenye maendeleo endelevu.


Na Mwandishi Wetu.

Babati, Manyara: Sherehe ya kumbukizi ya kuzaliwa ya Mkurugenzi wa Mati Super Brands Ltd, Bilionea David Mulokozi, imegeuka kuwa somo la upendo na kuthaminiana baada ya mkewe, Doreen Mulokozi, kumuandalia tukio la kushtukiza lililogusa wengi.

Katika sherehe hiyo iliyofanyika Babati Mjini na kuhudhuriwa na wageni mbalimbali waalikwa, Doreen alimzawadia mumewe zawadi mbili kubwa—ikiwa ni pamoja na kumualika mwanamuziki anayempenda, Banana Zoro, ambaye aling’ara jukwaani kwa burudani ya hali ya juu na kukonga nyoyo za mwenyeji wa hafla pamoja na wageni wote.


Mbali na burudani hiyo iliyoongeza shamrashamra katika tukio hilo, Doreen alimkabidhi mumewe gari kama zawadi maalum ya kumbukumbu ya siku yake ya kuzaliwa, hatua iliyodhihirisha mapenzi ya dhati na kuthamini mchango wake ndani ya familia.

Kwa upande wake, Banana Zoro alitoa shukrani zake za pekee kwa mwaliko huo, akieleza kuwa kushiriki katika hafla hiyo kumekuwa na maana kubwa kwake binafsi na kitaaluma.

Akizungumza kwa hisia na furaha, David Mulokozi alimshukuru mkewe kwa maandalizi hayo pamoja na zawadi ya kushtukiza, akieleza kuwa tukio hilo limekuwa moja ya kumbukumbu muhimu zaidi katika maisha yake.
“Kumbukizi yangu ya kuzaliwa alinifanyia mke wangu Doreen… kwangu vilikuwa vitu vya kipekee sana katika maisha yangu,” alisema Mulokozi.

Kwa utani, Mulokozi aliwataka pia wanawake wengine kuiga mfano huo kwa kuwapatia waume zao zawadi zenye thamani, badala ya zawadi ndogo ndogo za kawaida, jambo lililozua vicheko na furaha miongoni mwa wageni waliohudhuria.
Naye Doreen alimtakia mumewe baraka na mafanikio zaidi katika shughuli zake, huku akimuomba aitunze zawadi hiyo kama kumbukumbu muhimu ya upendo wao ili waendelee kuikumbuka hata watakapokuwa wazee.
Sherehe hiyo ilifanyika kwa mafanikio makubwa, ikijumuisha burudani, furaha na mshikamano wa kifamilia pamoja na marafiki, huku ikiakisi ujumbe mzito wa kuthaminiana, upendo wa kweli na umuhimu wa kusherehekea maisha pamoja.

 

MWANZA

Wadau wa Sekta ya Milki mkoani Mwanza wamesisitizwa kufanya kazi kwa weledi kwa kuzingatia sheria, taratibu na misingi ya taaluma ya milki ili kuhakikisha sekta hiyo inaendelea kutoa huduma bora na zenye kuaminika kwa wananchi.

Msisitizo huo umetolewa leo Machi 17, 2026 mkoani Mwanza na Kamishna wa Ardhi Msaidizi wa Mkoa huo, Bw. Wilson Luge, wakati akifunga kikao kazi cha wadau wa Sekta ya Milki kilichoandaliwa na Kitengo cha Milki kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.

Amesema mafunzo na semina zinazotolewa kwa wadau wa Sekta ya Milki yana mchango mkubwa katika kuongeza uelewa wa kitaalamu pamoja na kuimarisha utendaji kazi katika kutoa huduma bora kwa wananchi, hususan katika masuala yanayohusu tathmini ya mali na usimamizi wa milki.

“Tunapenda kuishukuru Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kupitia Kitengo cha Milki kwa kutoa semina na mafunzo kwa wadau wetu wa Sekta ya Milki. Mafunzo haya yatawasaidia kuongeza ujuzi na kuimarisha weledi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku,” amesema Luge.

Aidha, amewasisitiza wadau hao wa sekta ya milki kufanya kazi kwa kuzingatia maadili ya taaluma yao na kujiepusha na vitendo vinavyokiuka sheria ikiwemo kujihusisha na masuala ya utakatishaji fedha, huku akielezea umuhimu wa kufuata taratibu zote za kisheria na kitaaluma katika kutoaji huduma za tathmini ya mali.

Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kupitia Kitengo cha Milki (Real Estate) inaendesha mijadala ya pamoja na wadau kwa lengo la kupata maoni kuhusu utambuzi na usajili wa Wadau wa Sekta ya Milki ili kuboresha na kukuza sekta ya milki nchini.

Mijadala hiyo inalenga kutoa elimu, kubadilishana uzoefu na kujadili changamoto zinazoikabili sekta ya milki nchini ambapo tayari kitengo hicho kimefanya vikao vya mijadala katika mkoa wa Dar es Salaam, Arusha, Dodoma, Tanga, Mwanza na Morogoro.

Menejimenti ya Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) kwa kushirikiana na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) imebuni mfuko wa kushirikisha wadau (stakeholders) kuwezesha kusaidia matibabu ya Upandikizaji wa Viungo kwa kuanza na Upandikizaji Uloto kwa watoto wenye Selimundu(Sickle cell) na Upandikizaji Figo kwa Wananchi wenye Uhitaji. Akiwasilisha mpango huo kwenye mkutano wa Wenyeviti wa Bodi na Wakurugenzi wa Mashirika ambayo Serikali ina hisa ndogo (Miinority Interest Forum ) ulioandaliwa na ofisi ya Msajili wa Hazina, mjini Arusha, Mkurugenzi Mtendaji wa BMH ,Prof Abel Makubi ameeleza kuwa mfuko huo unajengwa kwa Dhana ya Wadau wenye Moyo wa Huruma wa kusaidia huduma za matibabu zenye gharama kubwa kwa Wananchi wenye uhitaji katika kuunga mkono juhudi za Serikali. Prof. Abel Makubi ameeleza kuwa mfuko huo unachangiwa na wadau kutoka mashirika ya umma chini ya uratibu ya Msajili wa Hazina, Mashirika Binafisi na mtu mmoja mmoja , na unategemewa kukusanya TZ shilingi billion 7 ndani ya miaka miwili ili kusaidia huduma hizo katika Matibabu, vifaa, kupanua miundombinu mbinu na kuendelea kujengea uwezo watalamu wa taaluma hizo.  

Mfuko huo unategemewa kuzinduliwa rasmi tarehe 8 Mei 2026 katika kilele cha Maadhimisho ya Miaka 10 ya BMH , na Wadau takribani 200 wameshirikishwa katika mpango huu .


Top News