Na Mwandishi wetu, Mtwara.


Serikali kupitia Ofisi ya Halmashauri ya Mtwara Mikindani imekabidhi vifaa saidizi na kiasi cha shilingi milioni 342 ikiwa ni jitihada ya kujikita katika utoaji wa mikopo isiyo na riba kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye Ulemavu.


Akizungumza katika hafla hiyo iliyofanyika Mkoani Mtwara, Mkindani leo tarehe 14/02/2026 Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) Mhe. Ummy Nderiananga, amesema hatua hiyo ni utekelezaji wa sera na mwelekeo wa maendeleo unaolenga kujenga uchumi jumuishi unaowawezesha wananchi wote kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji na maendeleo ya Taifa.

Naibu Waziri Ummy amefafanua, “Mikopo hii inalenga kuchochea na kuinua uchumi wa chini kwenda juu sambamba na mwelekeo wa dira ya Taifa ya kujenga uchumi shindani, jumuishi na endelevu ifikapo mwaka 2050.”

Ameongeza kuwa, utoaji wa vifaa saidizi ikiwemo viti mwendo, magongo, fimbo nyeupe za wasioona pamoja na taulo za kike, ni utekelezaji wa sera ya kutomwacha mtu nyuma katika safari ya maendeleo, sambamba na maono ya kitaifa ya kujenga jamii yenye heshima, utu na usawa wa fursa.

Kwa upande wake Mbunge wa jimbo la Mtwara Mjini na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana Mhe. Dkt. Joel Arthur Nanauka, ameweka wazi kuwa Serikali katika jitahada za kuwakwamua wananchi kiuchumi itaendelea na utekelezaji wa kuleta miradi mikubwa ya kimkakati katika Mkoa wa Mtwara ikiwemo kuboresha Bandari ya Mtwara, ujenzi wa reli, na uboreshaji wa uwanja wa ndege pamoja na marekebisho ya miundombinu ya Barabara.

Waziri Nanauka amehimiza, “Wanufaika wa mikopo hiyo kutumia fedha kwa malengo yaliyokusudiwa, na kurejesha kwa wakati ili kushirikiana katika kuhakikisha mikopo hiyo inaleta matokeo chanya kwao binafsi na Taifa kwa ujumla.”





Na Fatma Jalala

Licha ya Tanzania kuwa na mfumo madhubuti wa kisheria unaolenga kulinda na kukuza ushiriki wa makundi maalum katika ununuzi wa umma, ushahidi kutoka ngazi ya jamii unaonesha kuwepo kwa pengo kubwa kati ya kile kinachoahidiwa kupitia sera na uhalisia unaotokana na utekelezaji wa ahadi hizo.

Ukosefu wa elimu ya kutosha, unaelezwa kuwa ndio chanzo kikuu cha hali hiyo inayowakabili wajasiriamali kutoka makundi maalum, hususan wanawake.

Ingawa sheria inataka kutengwa kwa kiwango maalum cha ununuzi wa umma kwa kila taasisi kwa ajili ya makundi maalum, hilo halifanyiki na kuwanyima wajasiriamali hao kunufaika na fursa zinazopatikana kupiyia ununuzi wa umma.

Serikali imeweka mikakati mbalimbali ya kuinua makundi maalum kiuchumi kupitia Sheria ya Ununuzi wa Umma, ambayo inaelekeza kutengwa kwa asilimia 30 ya bajeti ya ununuzi wa umma kwa ajili ya makundi hayo. Lengo ni kuwapa fursa ya kupata zabuni, kukuza biashara ndogo ndogo, na hatimaye kuimarika kiuchumi.

Pamoja na kuwepo kwa sera na sheria hizo kwa muda mrefu, wanawake wengi katika Wilaya ya Kinondoni hawana uelewa wa kutosha kuhusu fursa hizo. Hali hiyo inasababisha kutowasilisha maombi ya zabuni, kushindwa kufikia vigezo vinavyohitajika, na hivyo kushindwa kunufaika na fursa zilizopo.

Mfumo wa kisheria na kikanuni

Sheria ya Ununuzi wa Umma ya mwaka 2023 ndiyo msingi mkuu wa taratibu za ununuzi wa bidhaa, huduma na kazi za ujenzi kwa taasisi za serikali. Sheria hii, pamoja na kanuni zake, inasisitiza umuhimu wa kutoa fursa maalum kwa makundi yaliyoainishwa.

Kwa mujibu wa Kifungu cha 64(1–2)(c), taasisi zote za ununuzi wa umma zinatakiwa kutenga angalau asilimia 30 ya thamani ya ununuzi wao wa mwaka kwa makundi maalum, yakiwemo wanawake, vijana, watu wenye ulemavu na wazee.

Aidha, Kanuni ya 30C ya Kanuni za Ununuzi wa Umma inaeleza umuhimu wa namna makundi maalum kusajiliwa na kuthibitishwa kwenye Mfumo wa Kitaifa wa Manunuzi (NeST) ili kuzipata fursa hizo.

Kwa mujibu wa mwongozo wa Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), mgawanyo huo wa asilimia 30 unakwenda kwa wanawake (asilimia 10), watu wenye ulemavu (asilimia 10), vijana (asilimia tano) na wazee (asilimia tano).

Changamoto ya uelewa ngazi ya jamii

Pamoja na sheria kuweka vigezo hivyo, kanuni na miongozo iliyo wazi, bado kuna changamoto kubwa ya uelewa miongoni mwa wanawake wilayani Kinondoni.

Baadhi ya wanawake wajasiriamali katika masoko ya Tandale na Magomeni wanasema hawajawahi kusikia wala kuelimishwa kuhusu mfumo wa NeST.

Kwa maana hiyo, hawafahamu fursa za ununuzi wa umma zilizotengwa kwa ajili yao.

Blandina Daniel (46), mama lishe na mweka hazina katika Soko la Tandale, anasema wanawake wengi hawajawahi kupata elimu kuhusu mfumo wa NeST wala ununuzi wa umma. Anaeleza kuwa waliwahi kuhamasishwa kuunda vikundi na kupata wataalamu kutoka BRELA, lakini jitihada hizo hazikuendelea na vikundi vikavunjika.

Theresia Paschal Joseph (44), mjasiriamali katika Soko la Magomeni, anasema maisha ya ujasiriamali yamekuwa yakitegemea mapato ya kila siku bila matarajio ya kupanua biashara kutokana na kukosa taarifa na fursa. Anaamini kuwa kama angepata elimu na uwezeshaji kupitia mifumo ya serikali, maisha yake yangekuwa tofauti.

Hali hii inaonyesha wazi kuwa tatizo kubwa si ukosefu wa sera au sheria, bali ni changamoto ya utekelezaji wa sheria hiyo hasa katika eneo la utoaji wa elimu kwa walengwa.

Kauli hizi zinaakisi uhalisia wa makundi maalum ambayo yanalindwa kisheria, lakini hayajafikiwa kielimu, hali inayodhoofisha dhamira ya sheria.

Athari za kijamii na kiuchumi

Delfina Ladslaus (38), mfanyabiashara wa mboga mboga katika Soko la Magomeni, anaeleza kuwa mara nyingi wanaambiwa kuhusu mikopo ya asilimia 10, lakini wanapoamua kufuatilia wanaishia kwenye hatua ya usajili bila kunufaika.

Kwa mujibu wa mfanyabiashara huyu, hali hii ina athari za kisaikolojia kwao.

Kwa upande mwingine, kauli za viongozi kwamba “kinamama wamewezeshwa” wakati uhalisia ni tofauti, husababisha kukata tamaa na kupoteza imani kwa serikali.

Mariam Tandu Kimea (52) anabainisha kuwa kukosa elimu na fursa huathiri zaidi wanawake, hasa wajane na wale wanaolea familia peke yao.

Hali hii husababisha kushindwa kumudu gharama za maisha kama ada za watoto na hivyo kuendeleza mzunguko wa umaskini.

Mitazamo ya viongozi wa ngazi za msingi

Baadhi ya viongozi wa ngazi za mitaa na kata pia wanaonesha kutokuwa na taarifa za kutosha kuhusu mfumo wa NeST.

Diwani wa Kata ya Tandale, Abdulaziz Said (45), anasema hajawahi kupata taarifa rasmi kuhusu elimu ya mfumo huo.

Mwenyekiti wa Soko la Tandale, Sultani Kiyumbo (58), naye anasema fursa hizo anazifahamu kwa juhudi binafsi, lakini hajawahi kuona elimu ikitolewa sokoni.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Soko la Magomeni, Daudi Dolle (64), anasema wanawake wengi hawajawahi kufikiwa na fursa hizo kutokana na kukosa elimu ya mfumo huo.

Uwepo wa sheria bila elimu ya utekelezaji

Kanuni za Ununuzi wa Umma, 2024 (GN Na. 518/2024), pamoja na miongozo ya PPRA, zinaweka mifumo ya uwazi, ushindani na upendeleo kwa makundi maalum. Pia, Sera ya Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi inalenga kutumia ununuzi wa umma kama chombo cha kuinua wanawake kiuchumi.

Hata hivyo, ripoti ya utendaji ya PPRA 2020-21, inayolezea tathmini ya utengaji wa asilimia 30 kupitia ukaguzi imebaini kuwa mambo ya msingi yaliyoainishwa kwenye sheria hayatekelezwi ipasavyo.

Sheria ya Ununuzi wa Umma inaitaka kila taasisi kutenga asilimia 30 ya bajeti yake ya ununuzi kwa ajili ya makundi maalum yaani wanawake, vijana, wazee na watu wenye ulemavu. PPRA ilifanya ukaguzi ili kupima endapo taasisi hizo zilitekeleza matakwa hayoya sheria.

Ukaguzi huu ulibaini kuwa kati ya taasisi 86 zilizofanyiwa tathmini, ni taasisi mbili tu zilizozingatia matakwa haya, taasisi tatu zilikuwa zimetenga pungufu ya asilimia 30, wakati taasisi 81 hazikuwa zimetenga chochote kwa ajili ya makundi maalum.

Aliyekuwa Waziri wa Fedha, Dkt. Mwigulu Nchemba, akizitaka taasisi za umma kutumia kikamilifu mfumo wa ununuzi wa umma kielektroniki (NeST) akisisitiza kuwa “mifumo haina mbadala.”

Naye Afisa Ununuzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni, Vumilia Tigwela, anakiri kuwepo kwa changamoto ya elimu na ufuatiliaji. Anasema sababu kuu ni pamoja na ukosefu wa mafunzo maalum, kampeni hafifu za uelimishaji, na changamoto za kiufundi katika matumizi ya mfumo wa NeST.

Kwa mwaka wa fedha 2024/25, Halmashauri ilifanya ununuzi wa takribani shilingi bilioni 50, ambapo wastani wa shilingi bilioni mbili pekee ziliwanufaisha makundi maalum.

Wajibu wa taasisi

Meneja wa PPRA Kanda ya Pwani, Vicky Mollel, anasema mamlaka hiyo inafuatilia utoaji wa elimu kupitia Halmashauri mbalimbali.

Hata hivyo, changamoto kubwa ni mwitikio mdogo wa walengwa na ukosefu wa ufuatiliaji wa mafunzo yanayotolewa.

Uhalisia unaonesha kuwa makundi maalum yanaendelea kubaki kuwa watazamaji wa sera zinazowahusu, badala ya kuwa washiriki.

Hali hiyo inahatarisha lengo la ununuzi wa umma kama chombo cha uwezeshaji wa kiuchumi na maendeleo jumuishi.

Bila uwekezaji mkubwa katika elimu ya mfumo wa NeST na fursa za ununuzi wa umma, dhamira ya sheria na sera zilizopo itaendelea kubaki kwenye maandishi badala ya kubadilisha maisha ya wananchi.

- Ni ili Kupunguza Ugonjwa wa Selimundu

Na Karama Kenyunko Michuzi Tv

KUPIMA vinasaba kabla ya kuingia kwenye mahusiano imeelezwa kuwa ni njia sahihi ya kuzuia kuongezeko la watoto wanaozaliwa na ugonjwa wa selimundu nchini.

Hayo yameelezwa leo Februari 14, 2026 na Dkt. Elisha Osati,kutoka Shirikisho la Vyama vya Ugonjwa wa Selimundu Tanzania wakati wa kumtambulisha Miss Tanzania mwaka 2018, Elizabeth Makune, kama balozi wa ugonjwa huo atakayeongoza Kamepeni ya 'Vunja Mduar.'

Dkt. Osati ambaye pia ni Mwenyekiti wa Mtandao wa Wataalamu wa Kupambana na Ugonjwa wa Selimundu Tanzania (TSDA),amesema kila mwaka watoto 11,000 hadi 14,000 wanazaliwa wakiwa na ugonjwa wa selimundu (sickle cell).

Amesema ugonjwa wa sickle cell upo katika kila nchi, japo haujatambuliwa kwa kiasi kikubwa.

Amesema Tanzania ni ya nne Afrika na ya tano duniani kwa kuwa na ugonjwa huo, ukiacha India na Nigeria na nchi nyingine.

“Kila mwaka tunakadiria watoto 11,000 hadi 14,000 wanazaliwa wakiwa na ugonjwa huu na ukiangalia takwimu hizi ni wazi zinashangaza kwani ni asilimia 0.1 hadi 0.2 ya Watanzania wana sickle cell, ugonjwa ambao unapatikana kwa kurithi kutoka kwa mzazi mmoja na mwingine,” amesema.

Amesema wamekuwa wakifanya tafiti mbalimbali ikiwemo kutibu wagonjwa na kujionea ukubwa wa tatizo hilo na ndiyo maana wameamua kwenda kwa jamii kuonyesha ukubwa wa tatizo na kujua namna ya kuzuia ugonjwa usiongezeke.

“Huu ni ugonjwa unaosababisha upungufu wa damu pamoja na maumivu makali mwilini, manjano na homa za mara kwa mara, hivyo kufanya mtoto kushindwa kuendelea na masomo yake, lakini mzazi kushindwa kuendelea na shughuli za uzalishaji kiuchumi kutokana na kuchukua muda mwingi kumhudumia mtoto anayeugua mara kwa mara,” amesema.

Amesema wataalamu wamekaa pamoja kwa ajili ya kutafuta suluhisho.

Amesema gharama za kutibu ugonjwa wa selimundu ni kubwa kiasi kinachofikia dola milioni mbili, hivyo wamekuja na njia ya kuzuia mtoto asipate ugonjwa huo kwa kuwaasa vijana kabla ya kuingia kwenye mahusiano kupima vinasaba ili wajue kama wanaweza kuendelea na mahusiano au la.

Naye Mtendaji Mkuu wa shirikisho hilo, Dkt. Soka Deogratius, amesema wanataka kutoa zawadi kwa Watanzania kwa kuongeza uelewa wa afya ili waweze kuanza na familia bora.

Kwa upande wake, balozi wa kampeni ya Vunja mduara, Elizabeth Makune amesema ugonjwa wa selimundu kwa jamii ya Kitanzania ni mwiko na wengine wanakwenda mbali zaidi na kuhusisha ugonjwa huo na laana au imani za kishirikina.

“Ni wazi mahali palipo na mwiko kuna ukimya na penye ukimya kuna vifo vinavyoweza kuzuilika. Japokuwa ugonjwa huu una gharama kubwa na ni mzigo kwa familia na taifa kwa ujumla,” amesema.

Ameongeza kuwa Mtanzania wa kawaida hawezi kumudu gharama ya Sh milioni mbili kwa ajili ya matibabu.

Amesema kwa nchi kama Tanzania njia pekee na ya busara zaidi si tiba bali ni kinga.

“Tuwe wakweli, huduma ya upandikizaji uloto imeanza kutolewa mwaka 2023 katika Hospitali ya Benjamin Mkapa Dodoma, lakini ni watu wachache wanaweza kuitumia kwani hadi sasa ni wagonjwa 26 tu ndio walioweza kupata matibabu haya ambayo yanaweza kugharimu hadi Sh milioni 75, hivyo ni wazi hili si suluhisho,” amesema.

Amesema watoto wenye umri wa chini ya miaka miwili hufariki kutokana na ugonjwa wa Selimundu kwa sababu wa uelewa mdogo wa familia wa kulitambua tatizo mapema.

Mwanzilishi wa Selimundu Family, Erick Ndikilo, amesema amefurahi kuungana na wenzake katika mapambano hayo, akisema yeye kama muathirika wa ugonjwa huo kwa miaka 30 sasa amepitia changamoto za kiafya.

“Mtanzania anayetusikiliza asiyefahamu, selimundu ni ugonjwa kama ugonjwa mwingine na kama mtu akiuelewa na kufuatilia matibabu basi mtu anaweza kuishi maisha marefu,” amesema
Balozi wa kampeni ya 'vunja mduara'  juu ya ugonjwa wa Selimundu, Elizabeth Mkune ambaye pia ni Miss Tanzania 2018, akizungumza na waandishi wa habari leo Februari 14, 2026 jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa shirikisho la vyama vya ugonjwa wa Selimundu Dkt. Deogratius Soka (kushoto) akizungumza leo Februari 14, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa kumtambulisha Miss Tanzania mwaka 2018, Elizabeth Makune (hayupo pichani) kama balozi wa  kampeni ya 'Vunja Mduara' juu ya ugonjwa wa Selimundu nchini . Pembeni yake ni Mwenyekiti Shirikisho la Vyama vyama vya ugonjwa huo Dkt. Elisha Osati.

Mkurugenzi Mkuu wa TASAC Mohamed Salum na Mwakilishi wa Kudumu wa Liberia katika IMO, Balozi  Wilmot Kpadeh wakionesha hati za makubaliano ya  ushirikiano kati ya Tanzania na Nchi ya Libaria kwa katika masuala ya usafirishaji kwa njia ya Bahari ,jijini Dar es Salaam.

Na Mwandishi Wetu
TANZANIA imepiga hatua kubwa katika safari ya kuwa kitovu cha usafiri wa majini katika ukanda wa Afrika Mashariki baada ya kusaini Hati ya Makubaliano (MOU) ya kihistoria na nchi ya Liberia, yenye lengo la kuimarisha ushirikiano katika usajili wa meli, mafunzo kwa mabaharia na usimamizi wa sekta ya bahari.

Makubaliano hayo yalisainiwa jana katika hafla iliyohudhuriwa na viongozi wa juu wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania Tanzania (TASAC) pamoja na Mamlaka ya Bahari Liberia (LiMA) nchini Liberia, mashirikiano hayo yakitajwa kuwa hatua muhimu katika kukuza uchumi wa buluu barani Afrika.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa TASAC, Mohamed Salum, alisema makubaliano hayo si ya ishara tu bali ni mfumo rasmi wa ushirikiano wa vitendo.

“Huu ni mfumo uliopangwa kwa ajili ya kuimarisha usimamizi wa sekta ya bahari, kujenga uwezo wa rasilimali watu na kuweka kanuni zinazoendana na mwelekeo wa dunia,” alisema.

Amesema kuwa uzoefu wa Liberia kama kinara wa Kimataifa katika usajili wa meli na usimamizi wa viwango vya kimataifa utatoa fursa ya kipekee kwa Tanzania kuimarisha daftari lake la kimataifa la usajili wa meli pamoja na kuongeza ubora wa wataalamu wake wa baharini.

Amesema nchi ya Liberia ina uzoefu wa miongo kadhaa katika usafirishaji wa kimataifa na ushiriki wake katika International Maritime Organization (IMO).

Kupitia makubaliano hayo TASAC watanufaika na programu za kubadilishana uzoefu, mafunzo ya kitaalamu pamoja na fursa za kupata vyeti vinavyotambulika kimataifa, vitakavyowawezesha kufanya kazi katika meli zilizosajiliwa chini ya bendera ya Liberia.

Mwakilishi wa Kudumu wa Liberia katika IMO, Wilmot Kpadeh, alisema makubaliano hayo ni hatua ya kihistoria itakayojenga urithi wa kudumu kwa mataifa hayo mawili.

“MOU hii inaweka msingi wa urithi ambao vizazi vijavyo vitauthamini. Afrika inachangia asilimia nne tu ya mabaharia milioni 1.9 duniani licha ya kuwa na ukanda mrefu wa pwani. Kupitia ushirikiano huu, tunaweza kufundisha, kuthibitisha na kuwawezesha wataalamu wapya wa bahari kutoka Afrika,” alisema.

Aidha, ushirikiano huo utaipa Tanzania nafasi ya kunufaika na uzoefu wa Liberia katika ushiriki wa shughuli za IMO. Ingawa Tanzania si mjumbe wa Baraza la IMO, makubaliano hayo yataiwezesha kushiriki katika uwasilishaji wa hoja na mijadala ya sera katika ngazi ya kimataifa.
Mkurugenzi Mkuu wa TASAC Mohamed Salum (kushoto)akimpa zawadi   Mwakilishi wa Kudumu wa Liberia katika IMO, Balozi  Wilmot Kpadeh mara baada ya kusaini  hati za makubaliano ya  ushirikiano kati ya Tanzania na Nchi ya Libaria kwa katika masuala ya usafirishaji kwa njia ya Bahari ,jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mkuu wa TASAC Mohamed Salum  Akizungumza na waandishi wa habari mara  baada ya kusaini makubaliano ya Ushiriakiano na  Mamlaka ya Bahari ya nchini Liberia (LiMA) katika hafla uliyofanyika jijini Dar es Salaam.


Picha za mukundi mbalimbali mara baada ya kuhitimisha utiaji saini ya hati ya makubaliano kati ya Tanzania na Liberia katika eneo la usafirishaji kwa njia ya Bahari  jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mkuu wa TASAC Mohamed Salum na Mwakilishi wa Kudumu wa Liberia katika IMO, Balozi  Wilmot Kpadeh wakisaini hati ya makubaliano ya ushirikiano kati ya Tanzania na Nchi ya Libaria kwa katika masuala ya usafirishaji kwa njia ya Bahari ,jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mkuu wa TASAC Mohamed Salum  Akizungumza mara baada ya kusaini makubaliano na Mamlaka ya Bahari ya nchini Liberia (LiMA) katika hafla uliyofanyika jijini Dar es Salaam.




UN Tourism imeitaja Tanzania kushika nafasi ya 11 duniani na nafasi ya sita (6) kwa Afrika na Mashariki ya Kati na kuwa miongoni mwa nchi 20 katika nchi zilizofanya vizuri zaidi katika sekta ya Utalii duniani. 

Ripoti ya Januari 2026 iliyotolewa na UN Tourism  imeangalia ongezeko la watalii wa Kimataifa kati ya mwaka 2019 na 2025.

NA MASHAKA MHANDO, Korogwe

WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, amemwagiza Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga (RPC), ACP Almachius Mchunguzi, kumsaka na kumkamata mkandarasi aliyekimbia baada ya kulipwa Shilingi Milioni 934 kwa ajili ya ukarabati wa mradi wa maji katika mji wa Mombo, wilayani Korogwe.

Dkt. Mwigulu ametoa agizo hilo Leo February 14 mara baada ya kukagua mradi wa maji wa Miji 28 unaotekelezwa katika wilaya nne za mkoa wa Tanga, ambapo ameeleza kukerwa na mkandarasi huyo aliyepokea fedha za umma na kutoweka bila kutekeleza mradi, huku wananchi wakiendelea kutaabika na ukosefu wa maji.

"Ameondoka na fedha wakati wananchi wanapata shida; haya ndiyo mambo yanayokera na kuchukiza. RPC, huyu mtu atafutwe popote alipo, akamatwe na awekwe ndani mpaka arejeshe fedha za umma. Sijateuliwa ili nipendwe, na sitakuwa na huruma na watu wanaohujumu miradi ya Serikali," alisisitiza Waziri Mkuu.

Mradi wa Miji 28 Kufikia Asilimia 75

Mapema, Waziri wa Maji, Mhe. Jumaa Aweso, alimweleza Waziri Mkuu kuwa mradi wa maji wa Miji 28 unaogharimu Shilingi Bilioni 171 umefikia asilimia 74 ya utekelezaji wake. Mradi huo unatarajiwa kuwa ukombozi kwa wakazi wa wilaya za Korogwe, Handeni, Muheza, na Pangani.

Waziri Aweso alibainisha kuwa mradi huo utazalisha lita milioni 52 za maji kwa siku, zitakazohudumia wananchi wapatao 860,000 katika vijiji 161. Alimshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha hizo na kueleza kuwa mradi unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Machi, 2026.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ametoa maelekezo ya haraka kwa wataalamu wa maji kuhakikisha wananchi wa Kijiji cha Tabora, Kata ya Mswaha (Korogwe Vijijini), ambao mradi unapita katika maeneo yao, wanapatiwa huduma ya maji mara moja ili nao wanufaike na matunda ya uwekezaji huo mkubwa.

Dkt. Mwigulu alihitimisha kwa kusema kuwa Serikali itaendelea kuwa na msimamo mkali dhidi ya mkandarasi yeyote atakayefanya kazi chini ya kiwango au kuiba fedha za miradi, akisisitiza kuwa thamani ya fedha lazima ionekane kwa wananchi.

Mapema asubuhi Waziri Mkuu akiwa wilayani Kilindi  ametoa onyo kali kwa wasimamizi wa ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Kilindi, akisema atachukua hatua kali za kinidhamu na kisheria endapo itabainika kuwepo kwa ubadhirifu wa Shilingi Bilioni 2.6 zilizotolewa kwa ajili ya mradi huo.

Dkt. Mwigulu ametoa kauli hiyo mara baada ya kuweka jiwe la msingi la hospitali hiyo, ambapo licha ya kuridhishwa na ubora wa majengo yaliyokamilika, ameshitushwa na taarifa za kutoonekana kwa jengo la wodi ya mama na mtoto wakati fedha zake zilikwishatolewa na Serikali.

"Nimekuja kuweka jiwe la msingi baada ya kuridhishwa na viwango vya ujenzi wa majengo haya, lakini DED nimeambiwa fedha iliyokuja ilitakiwa ijenge majengo mengi zaidi ya haya. Nyinyi mmejenga majengo pungufu, fedha nyingine mmeipeleka wapi?" alihoji Waziri Mkuu.

Sakata la Saruji ya Mbeya na "Kichaka" cha Gharama.

Waziri Mkuu amefichua mchezo unaofanywa na baadhi ya watumishi wa kuhalalisha matumizi mabaya ya fedha kwa kununua vifaa vya ujenzi mbali na maeneo ya mradi ili kuongeza gharama za usafirishaji. Ameshitushwa na taarifa kuwa saruji ya ujenzi wa hospitali hiyo imenunuliwa mkoani Mbeya badala ya kutumia viwanda vya saruji vilivyopo jirani mkoani Tanga.

"Kuna mchezo unataka kuhalalishwa hapa wa kununua vifaa mbali; najua saruji mmenunua Mbeya. Takukuru fuatilieni kila kitu kwenye hiki kichaka cha gharama ili niweze kuchukua hatua kali. Hatuwezi kuwavumilia watu wanaoisababishia Serikali hasara kiasi hiki," alisisitiza.

Mapema, John Mgalula Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi (DED), alikiri mbele ya Waziri Mkuu kuwa fedha zilipokelewa kwa ajili ya majengo tisa, lakini majengo ya kufulia na kutolea dawa hayajakamilika kutokana na kile alichodai kuwa ni kuongezeka kwa gharama za kusafirisha vifaa.

Mgogoro wa mpaka kati ya Simanjiro na Kilindi

Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu amechukua hatua za haraka kutatua mgogoro wa mpaka kati ya wilaya za Simanjiro (Manyara) na Kilindi (Tanga), ambao umedumu kwa muda mrefu na kusababisha mivutano kati ya wakulima na wafugaji.

Waziri Mkuu ametangaza kuunda Kamati ya Mawaziri wa Kisekta itakayojumuisha Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Maliasili na Utalii, pamoja na TAMISEMI ili kumaliza kabisa mgogoro huo na kurejesha amani katika maeneo ya mipakani.

Kikao hicho kitakutana mkoani Tanga February 16 kabla Waziri Mkuu hajaondoka mkoani hapa kuelekea mkoani kilimanjaro













 

NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Taasisi isiyo ya kiserikali, Kaya Foundation, imekabidhi msaada wa viti mwendo vitano vilivyotolewa na Ubalozi wa Ufaransa nchini Tanzania, pamoja na bima za afya kwa watoto wenye changamoto ya ulemavu, hatua inayolenga kupunguza vikwazo katika makuzi na elimu yao.

Akizungumza katika hafla ya makabidhiano iliyofanyika leo Februari 14, 2026 jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa Kaya Foundation, Pili Ana Ngome, amesema taasisi hiyo imetoa viti mwendo vitano na kugharamia bima za afya kwa watoto 12 kupitia michango ya wananchi.

Amesema msaada huo unalenga kuwezesha watoto wenye ulemavu kuhudhuria shule kwa urahisi, akibainisha kuwa wengi wao wamekuwa wakikosa fursa ya elimu kutokana na ukosefu wa vifaa saidizi.

“Tumetoa msaada huu ili kuhakikisha watoto hawa wanapata haki yao ya msingi ya elimu. Viti mwendo vitawasaidia kufika shule na kushiriki kikamilifu katika masomo,” amesema.

Aidha, Ngome ametoa wito kwa jamii kujitokeza kuchangia ustawi wa watoto wenye ulemavu kwa kuwapatia bima za afya, akisisitiza kuwa uwekezaji huo utasaidia Taifa kupata wataalamu na wasomi wa baadaye.

“Lengo letu kuu ni kuhakikisha watoto wenye ulemavu wanapata elimu kama watoto wengine. Tusipowasaidia, Taifa litapoteza rasilimali watu muhimu,” ameongeza.

Kwa upande wake, Diwani wa Viti Maalumu wa Jiji la Dar es Salaam, Julieth Baingwa, ameipongeza Kaya Foundation kwa jitihada zake, akisema taasisi hiyo imekuwa mstari wa mbele katika kushughulikia changamoto za watoto wenye ulemavu.

Naye mzazi wa mtoto aliyenufaika na msaada huo, Tatu Said Salum, ameishukuru taasisi hiyo akieleza kuwa kiti mwendo kitamwezesha mtoto wake kurejea shuleni.

“Mwanangu alishindwa kuendelea na masomo kwa kukosa kiti mwendo. Sasa ataweza kurudi shule na kuendelea na ndoto zake,” amesema.






Kikundi cha Kinamama Kihesa kilichoanzishwa mwaka 2008 leo kimeadhimisha Siku ya Wapendanao kwa kufanya sherehe ya pamoja na kutembelea Shule ya Viziwi ya Iringa ambapo wametoa zawadi mbalimbali kwa wanafunzi na walezi wao.

Akizungumza katika hafla hiyo Mwenyekiti wa kikundi hicho Upendo Makasi amewashukuru wanachama kwa kuendelea kudumisha umoja na mshikamano tangu kuanzishwa kwa kikundi hicho mwaka 2008. 

Amesema kwa miaka yote wamekuwa wakijitoa katika shughuli mbalimbali za kijamii zenye lengo la kusaidia makundi yenye uhitaji maalum.

Ametoa wito kwa jamii kuendelea kujitolea na kusaidia watu wenye changamoto mbalimbali akisisitiza kuwa upendo wa kweli unaonekana kupitia matendo.

Kwa upande wake Kaimu Mkuu wa Shule ya Viziwi Iringa Abraham Moses amesema shule hiyo inapokea wanafunzi kutoka mikoa mbalimbali nchini Tanzania. 

Ameeleza kuwa wanafunzi hao wanahitaji upendo na mazingira bora ya kujifunzia ili waweze kutimiza ndoto zao.

Amesema shule hiyo ina jumla ya wanafunzi 120 kuanzia darasa la kwanza hadi la saba huku muda wa masomo ukitofautiana kulingana na mahitaji maalum ya wanafunzi ambapo baadhi yao huchukua hadi miaka saba au zaidi kukamilisha mzunguko wa elimu ya msingi.

Aidha ametaja changamoto ya afya kuwa ni kubwa akisema wanafunzi wanapougua hukosa huduma za matibabu kwa wakati kutokana na ukosefu wa bima za afya. 

Amesisitiza umuhimu wa kupatiwa bima za afya kwa wanafunzi hao ili kupunguza gharama kubwa za matibabu.

Pia ameeleza kuwa shule inakabiliwa na changamoto ya usafiri, kwani gari lililopo ni bovu na haliwezi kutumika ipasavyo wakati wa dharura au shughuli mbalimbali za shule.

Vilevile, amesema kuna baadhi ya wazazi huwapeleka watoto wao shuleni hapo lakini hawarudi tena kuwasalimia wala kuwachukua hali inayosababisha mzigo mkubwa wa malezi na gharama kubaki kwa shule.

Naye Mwakilishi wa Afisa Maendeleo ya Jamii Kata ya Kihesa Mwl. Grace Sanga, amewashukuru kinamama hao kwa moyo wao wa kujitolea. 

Amesema Serikali inaendelea kutekeleza mipango mbalimbali ya maendeleo kwa jamii na ushiriki wa wadau katika kuongeza nguvu ni jambo la kupongezwa na kuungwa mkono.







 


Top News