Benki Kuu ya Tanzania (BoT), ikiongozwa na Naibu Gavana wa Sera za Uchumi na Fedha, Dkt. Yamungu Kayandabila, imefanya kikao na wadau mbalimbali kujadiliana kuhusu mpango wa kuanzishwa kwa kampuni ya utoaji na usimamizi wa dhamana za mikopo itakayojulikana kama Tanzania Credit Guarantee PLC.

Kikao hicho kilichofanyika leo, tarehe 12 Machi 2026, katika ofisi za Benki Kuu jijini Dar es Salaam, kimewakutanisha wadau kutoka taasisi mbalimbali ikiwemo Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA), Kampuni za Bima, Mifuko ya Pamoja ya Uwekezaji wa Mitaji, Mifuko ya Pensheni pamoja na Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF).

Mpango wa kuanzishwa kwa kampuni hiyo unalenga kuendana na ukubwa na kasi ya utekelezaji unaohitajika kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambayo inalenga kuimarisha uchumi wa Tanzania na kuongeza mchango wa sekta binafsi katika maendeleo ya taifa.

Vilevile, kampuni hiyo itasaidia kutenganisha majukumu ya Benki Kuu ya udhibiti na utoaji wa dhamana za mikopo, hivyo kuondoa mgongano wa maslahi na kuboresha ufanisi wa kiutendaji. Pia itahamasisha ubunifu pamoja na kuongeza uwezo wa taasisi husika kujibu kwa haraka mahitaji ya soko.

Kwa sasa, Benki Kuu ya Tanzania inasimamia mifuko miwili ya udhamini wa mikopo ambayo ni Mfuko wa Udhamini wa Mikopo kwa Mauzo ya Nje (Export Credit Guarantee Scheme – ECGS) na Mfuko wa Udhamini wa Mikopo kwa Wajasiriamali Wadogo na wa Kati (SME Credit Guarantee Scheme – SME-CGS).

Serikali ilianzisha mifuko hiyo kwa lengo la kudhamini benki na taasisi za fedha ili kuimarisha utoaji wa mikopo kwa wakopaji wenye miradi yenye tija lakini wanaokabiliwa na upungufu wa dhamana. Lengo kuu ni kuwezesha mazingira rafiki ya kukuza na kuendeleza miradi ya maendeleo, kuongeza ajira, kuimarisha upatikanaji wa fedha za kigeni kupitia mauzo ya nje na kuchangia ukuaji wa pato la Taifa.
Naibu Gavana, Dkt. Yamungu Kayandabila, akielezea jambo katika kikao na wadau kilichofanyika Benki Kuu jijini Dar es Salaam tarehe 12 Machi 2026.
Wadau mbalimbali katika kikao na Benki Kuu kilichofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 12 Machi 2026.
Mkurugenzi wa Ustawi na Huduma Jumuishi za Fedha BoT, Bw. Kennedy Komba, akifafanua jambo katika kikao na wadau kilichofanyika Benki Kuu jijini Dar es Salaam tarehe 12 Machi 2026.
Meneja wa Idara ya Huduma za Wakala wa Serikali BoT, Bw. Sadick Nyanzowa, akizungumza katika kikao na wadau kilichofanyika Benki Kuu jijini Dar es Salaam tarehe 12 Machi 2026.
Kamishna wa Bima Tanzania, Dkt. Baghayo Abdallah Saqware, akichangia mada katika kikao na wadau kilichofanyika Benki Kuu jijini Dar es Salaam tarehe 12 Machi 2026.
Afisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), CPA Nicodemus Mkama, akichangia mada katika kikao na wadau kilichofanyika Benki Kuu jijini Dar es Salaam tarehe 12 Machi 2026.
Naibu Gavana, Dkt. Yamungu Kayandabila pamoja na wadau baada ya kikao kilichofanyika Benki Kuu jijini Dar es Salaam tarehe 12 Machi 2026.

 Airtel Tanzania, kampuni inayoongoza huduma za mawasiliano nchini, imezindua maduka mapya 17 ya Airtel Smart Shops jijini Dar es Salaam. Maduka haya ni sehemu ya mtandao wa maduka 31 nchini kote, ukiwa na lengo la kupanua huduma za kidijitali na kuongeza ujumuishaji wa kifedha kwa wananchi.


Uzinduzi huo uliofanyika Machi 12, 2026, ulihudhuriwa na Mhe. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki, Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, pamoja na viongozi wa serikali, wajasiriamali, na vyombo vya habari.

Waziri Kairuki alieleza kuwa uwekezaji huu ni ishara ya nia ya dhati kwa Airtel kuleta mapinduzi makubwa katika sekta ya mawasiliano na kuonyesha imani yake katika mazingira ya biashara Tanzania chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.

“Maduka haya mapya yanaonyesha dhati ya Airtel katika kuleta huduma karibu na wananchi huku yakiboresha uzoefu wa wateja. Pia unaashiria imani thabiti katika mazingira ya biashara Tanzania,” alisema Waziri Kairuki.


Kwa upande wake, Charles Kamoto, Mkurugenzi Mtendaji wa Airtel Tanzania, alisema maduka haya hayako tu kama maduka ya rejareja. Yameundwa kama vituo vya kisasa vya huduma za kidijitali, vinavyotoa usajili wa SIM, intaneti ya kasi, huduma za kifedha kupitia Airtel Money, mauzo ya simu, na suluhisho za kibiashara kwa SMEs.


Maduka haya yamewekwa katika maeneo yenye shughuli nyingi jijini Dar es Salaam, ili kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wakazi na wajasiriamali. Uzinduzi huu ni sehemu ya mpango wa kitaifa wa “Airtel Kila Kona”, unaolenga kufanikisha upatikanaji wa huduma za mawasiliano hata katika maeneo ya vijijini.

Kampuni pia imewekeza katika kupanua mtandao wake wa 4G, kuanzisha teknolojia ya 5G, na kuongeza uunganishaji wa kimataifa kupitia mfumo wa nyaya za chini ya bahari wa 2Africa Submarine Cable System.



Adriana Lyamba, Mkurugenzi wa Uzoefu wa Wateja Airtel Tanzania, alisema maduka haya yameundwa kutoa huduma haraka, bila karatasi, na kwa ufanisi. Maduka haya yanatarajiwa pia kuunda ajira na kusaidia SMEs na wajasiriamali wa ndani kwa kuwapatia zana za kifedha za kidijitali na huduma za mawasiliano za kisasa.

Na Maandishi Wetu 

MKURUGENZI  Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi, Hassan Saidy amesema Wananchi hususan wanaoishi vijijini wana matumaini na Serikali kupitia REA katika kuwaboreshea hali ya maisha na amewataka Watumishi wa Wakala kuhakikisha wanafanya kazi kwa bidii, uadilifu na maarifa ili kutimiza malengo ya Serikali kuhudumia wananchi wake.

Ametoa rai hiyo Machi 12, 2026 mkoani Morogoro wakati wa kufungua Kikao cha Tatu cha Baraza la Pili la Wafanyakazi wa REA lenye ajenda kuu ya kupitia na kujadili mapato na matumizi kwa Mwaka 2026/2027.

"Watumishi wenzangu mnafanya kazi nzuri, tuendelee kuhakikisha tunawatumikia wananchi, matumaini yao kwetu ni makubwa na leo hii tupo hapa kujadili Mapato na Matumizi katika kutekeleza na kukamilisha miradi na kwa bajeti ya REA imezingatia vipaumbele vya Serikali ikiwemo kuharakisha kupeleka umeme vitongojini, kuongeza idadi ya wateja na kutanua wigo upatikanaji wa Nishati Safi ya Kupikia,” amesema Mhandisi Saidy.

Amesema makadirio ya Mapato na Matumizi ya Bajeti kwa Mwaka 2026/2027 yanayojadiliwa katika Baraza hilo yamelenga kuboresha mazingira ya kazi na uwezo wa Taasisi katika kutekeleza majukumu yake sambamba na maslahi ya Watumishi.

Akizungumzia mafanikio yaliyofikiwa ndani ya kipindi cha miezi 12 (kutoka kikao cha Baraza kilichopita cha Mwezi Machi, 2025 hadi kikao cha sasa Machi, 2026), Mha. Saidy amesema REA imefanikiwa kusambaza umeme kwenye vitongoji 3,532 ambayo ni sawa na wastani wa vitongoji 10 kwa siku.

"Ndani ya kipindi cha miezi 12 tumefanikiwa kusambaza mitungi 400,000, majiko banifu 300,000, kujenga mifumo ya kisasa ya kupikia kwa Taasisi 452 zinazohudumia zaidi ya Watu 100, tumeanza kutekeleza Mradi wa kupeleka Umeme - Jua kwa kaya takriban 20,000 katika visiwa 143 na ndani ya kipindi hiki miradi takriban mitatu ya kusambaza ùmeme imekamilika,” amesema Mkurugenzi Mkuu wa REA.

Akizungumza katika kikao hicho, Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE), Hery Mkunda ameipongeza REA kwa kuendelea kutekeleza majukumu yake kwa weledi na uzalendo.

“REA mnafanya kazi kubwa sana, mmefanikisha azma ya Serikali ya kubadilisha na kuboresha maisha ya wananchi wa maeneo ya vijijini, kwa hili kila mwananchi anaetoka kijijini ni shahidi,” amepongeza Mkunda.

Kikao cha Tatu cha Baraza la Pili la Wafanyakazi wa REA kilihudhuriwa na Mwakilishi wa Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Wilson Nyamanga, Mwakilishi wa Msajili wa HAZINA, Gerald Nzalalila pamoja na Katibu Mkuu wa TUGHE mkoa wa Dodoma, Samwel Nyangwa ambao walipata fursa ya kuzungumza na Watumishi.








Serikali kupitia Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) imejipanga kuhakikisha matumizi ya Nishati Safi ya kupikia  kupitia mradi wa Rafiki Briquete yanaongezeka katika mikoa mbalimbali nchini ili kufikia asilimia 86 ya matumizi ya  Nishati Safi ifikapo mwaka 2030.


Hayo yameelezwa leo Machi 12, 2026 Mkoani Tabora na Naibu Waziri wa Madini Dkt. Steven Kiruswa, wakati akitoa taarifa kwa Kamati ya Kudumu ya  Bunge ya Nishati na Madini ilipokuwa ikikagua miradi inayosimamiwa na Wizara ya Madini.

Dkt. Kiruswa amesema kuwa, STAMICO  tayari imeshanunua Mitambo minne yenye uwezo wa  kuzalisha tani 20 kwa saa ambayo imesimikwa katika  maeneo  ya Kiwira,  Pwani, Chigongwe Mkoani Dodoma na   Kiloleni Mkoani Tabora.

Dkt. Kiruswa amefafanua kuwa, kwa Mkoa wa Tabora, STAMICO imelenga kuhamasisha matumizi ya Nishati Safi kwa  wakulima wa Tumbaku ambao kwa muda mrefu  wamekuwa wakitumia kuni kwa wingi suala linalohusisha uharibifu  wa mazingira. 

Kwa upande wake  Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Nishati na Madini, Subira Mgalu  ameipongeza STAMICO kwa ubunifu wa miradi endelevu  yakimkakati  inayoleta mchango mkubwa kwa taifa ikiwa pamoja na  kuunganisha mnyororo mzima wa thamani madini.

Mgalu ameitaka STAMICO kuanza uzalishaji mapema  pamoja na  kufungua matawi mengine katika mikoa mbalimbali nchini ili kutekeleza Agenda ya kitaifa inayohusu  matumizi ya Nishati Safi ili kufikia  asilimia 86 za matumizi ya Nishati Safi ifikapo mwaka 2030.

Kwa upande wake  Msafiri Mbibo, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Madini , ameishukuru kamati kwa maoni mbalimbali yaliyolenga uboreshaji wa mradi huo hususan katika upande wa ajira na  Usimikaji wa mitambo ya Uzalishaji.

Awali, akitoa taarifa ya maendeleo ya mradi huo  Deusdedith  Magala, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji  wa STAMICO, amesema kuwa mradi wa Rafiki Briquettes katika Mikoa mbalimbali unatarajia kuajili watanzania zaidi ya 100




 





Na WMJJWM New York Marekani

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imesisitiza mshikamano wake na nchi wanachama wa jumuiya ya kimataifa katika kuendeleza ajenda ya usawa wa kijinsia duniani.

Akizungumza katika mkutano wa 70 wa kimataifa kuhusu masuala ya wanawake na haki, mwakilishi wa Tanzania katika Mkutano huo Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makuundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima amesema Tanzania inasisitiza kuwa upatikanaji wa haki ni msingi muhimu wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Aidha, amesema Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050 imeweka usawa wa kijinsia na ujumuishi wa kijamii kuwa nguzo kuu za ajenda ya maendeleo ya taifa, hali inayotumika kuongoza maboresho ya sheria na sera mbalimbali nchini.

Ameongeza kuwa Serikali imeendelea kutunga na kutekeleza sheria muhimu zinazolenga kulinda haki za wanawake na watoto wa kike. Baadhi ya sheria hizo ni pamoja na Sheria ya Ardhi, Sheria ya Msaada wa Kisheria, Sheria ya Ardhi ya Vijiji, Sheria ya Mtoto, Sheria ya Elimu pamoja na Kanuni ya Adhabu. Sambamba na hilo, mfumo wa mahakama umeimarishwa ambapo Tanzania imefanikiwa kupunguza kwa asilimia 50 mrundikano wa mashauri ya rufaa kati ya mwaka 2021 na 2024.

“Kupitia mageuzi ya kisheria, Tanzania imedhibiti mila na desturi zenye ubaguzi na kufanya marekebisho ya sheria mbalimbali ikiwemo Sheria za Uchaguzi ili kufanya unyanyasaji wa kijinsia katika siasa kuwa kosa la jinai. “amesema Dkt. Gwajima

Pia Dkt. Gwajima amesema Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeanzisha Mkakati wa Kitaifa wa Wanawake kupata Haki, Mkakati wa Pili wa Miaka Mitano wa Haki kwa Watoto, Mpango wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto, pamoja na Sera ya Taifa ya Ardhi inayohakikisha haki za wanawake kurithi ardhi huku juhudi zikiendelea kuimarishwa ili kutokomeza vitendo vya ukatili na mila potofu kama ukeketaji na ndoa za utotoni.

Dkt. Gwajima ameeleza kuwa katika kuboresha upatikanaji wa haki na kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma za sheria, Tanzania imeanzisha ubunifu mbalimbali ikiwemo mfumo wa usimamizi wa mashauri kwa njia ya kielektroniki (e-Case Management), Vituo Jumuishi vya Haki, pamoja na vituo maalum vya huduma za pamoja (One Stop Centres). Mwaka 2025, asilimia 88 ya mashauri katika vituo hivyo yalitatuliwa, huku wanawake wakichangia asilimia 61 ya wanufaika wa huduma za msaada wa kisheria.

Amefafanua kuwa kupitia Kampeni ya Kitaifa ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia, zaidi ya wanawake na wasichana milioni 2.1 Tanzania wamepatiwa msaada wa kisheria, elimu ya sheria pamoja na uwakilishi mahakamani.

Pamoja na mafanikio hayo, Tanzania imesisitiza kuwa bado kuna kazi kubwa ya kufanya katika kuhakikisha usawa wa kijinsia na upatikanaji wa haki kwa wote. Hivyo, imezitaka nchi na wadau wa maendeleo kuimarisha ushirikiano na ushirikishwaji ili kuendeleza ajenda ya kimataifa ya usawa wa kijinsia. Tanzania imeeleza kuwa iko tayari kujifunza kutoka kwa wengine na kushirikiana kwa pamoja katika kufanikisha lengo hilo duniani.









 

Benki ya Stanbic imeandaa futari maalum iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana, ikiwa ni sehemu ya kushiriki baraka za mwezi mtukufu wa Ramadan pamoja na kuimarisha mahusiano na wadau wake.

Tukio hilo liliwakutanisha viongozi wa dini, viongozi wa benki pamoja na wateja katika mazingira ya mshikamano na tafakari ya maadili ya kijamii yanayohimizwa katika kipindi hiki cha Ramadhani.

Mgeni rasmi katika hafla hiyo alikuwa Mufti Mkuu wa Tanzania, Abubakar Zubeir bin Ally, huku ujumbe wa Stanbic Bank ukiongozwa na Omari Mtiga, Mkuu wa Wateja Binafsi na Wateja Maalum wa benki hiyo.

Kupitia futari hiyo, Stanbic Bank ilisisitiza dhamira yake ya kuendelea kujenga mahusiano ya karibu na wadau wake huku ikiendeleza maadili ya heshima, mshikamano na utoaji kwa jamii. Tukio hilo pia lilitoa fursa kwa washiriki kubadilishana mawazo na kuimarisha ushirikiano unaochochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.
Omari Mtiga, Mkuu wa Wateja Binafsi na Wateja Maalum kutoka benki ya Stanbic Tanzania (katikati) akimkaribisha Mufti Mkuu wa Tanzania, Sheikh Dkt. Abubakar Zubeir bin Ally wakati wa futari maalum iliyoandaliwa na benki hiyo kwa wateja na viongozi wa dini katika Hoteli ya Serena, Dar es Salaam jana. Kulia ni Salim Abdallah Muhene. Tukio hilo lililenga kuimarisha mahusiano na wadau pamoja na kushiriki baraka za mwezi mtukufu wa Ramadhani.
Mufti Mkuu wa Tanzania, Sheikh Dkt. Abubakar Zubeir bin Ally, akipokea zawadi kutoka kwa Omari Mtiga, Mkuu wa Wateja Binafsi na Wateja Maalum, Stanbic Bank Tanzania, wakati wa futari maalum iliyoandaliwa na benki hiyo kwa wateja na viongozi wa dini katika Hoteli ya Serena, Dar es Salaam jana. Kulia ni Wilmont Ishengoma, Mkuu wa Tahadhari Stanbic Bank Tanzania. Tukio hilo lililenga kuimarisha mahusiano na wadau pamoja na kushiriki baraka za mwezi mtukufu wa Ramadhani.









Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amefanya mazungumzo na Balozi wa Cuba nchini Tanzania Mhe. Yordenis Despaigne Vera, mazungumzo yaliyofanyika Ikulu Chamwino Mkoani Dodoma, leo tarehe 12 Machi 2026.

Mazungumzo hayo, yamelenga kuimarisha uhusiano wa muda mrefu wa Tanzania na Cuba, ambao unatimiza miaka 64.  Cuba na Tanzania zimekuwa zikishirikiana katika Sekta mbalimbali za kimkakati kama vile Elimu, Afya, Utalii pamoja na Kilimo.

Tanzania na Cuba kwa miaka mingi zimeendelea kuwa na mahusiano na maelewano ya kiuchumi, kisiasa na kidiplomasia katika ngazi ya nchi mbili, kikanda na kimataifa. Tanzania na Cuba zilianzisha uhusiano wa kidiplomasia mwaka 1962 mara tu baada ya Tanzania kupata uhuru mwaka 1961.






Na Mwandishi Wetu

Ndoto ya kujikwamua kiuchumi kwa vijana wengi imepata mwanga mpya baada ya mkazi wa Dar es Salaam, Jerome Mushi, kujishindia pikipiki aina ya TVS kupitia promosheni ya “Shinda Boda” inayoendeshwa na kampuni ya michezo ya kubahatisha ya PigaBet Tanzania.

Mushi alisema ushindi huo ni fursa muhimu kwake na kwa kijana mwenzake kwani anapanga kuitumia pikipiki hiyo kuanzisha shughuli ya usafirishaji wa bodaboda ili kujiongezea kipato na pia kutoa ajira kwa kijana mwingine.

“Vijana wengi tunapambana mtaani ili kujikwamua kiuchumi, nami ni mmoja wao waliobahatika. Namshukuru Mungu kwa ushindi huu kwani utanisaidia pia kumfungulia fursa kijana mwenzangu aingie mtaani kufanya biashara ya bodaboda,” alisema Mushi.

Aliongeza kuwa amekuwa akishiriki mara kwa mara katika michezo hiyo na kupata ushindi mdogo mdogo, lakini safari hii amepata ushindi mkubwa ambao anaamini utabadilisha maisha yake.

Kwa upande wake, Afisa Masoko wa PigaBet Tanzania, Hemed Msonge, alisema promosheni ya “Shinda Boda” imeanzishwa kwa lengo la kuwainua Watanzania kiuchumi kwa kuwapatia zawadi za pikipiki.

Alisema katika promosheni hiyo kampuni hiyo inatoa pikipiki mbili kila wiki kwa kipindi cha wiki sita mfululizo kwa washindi wanaoshiriki katika michezo yake.

Msonge aliwahimiza Watanzania kushiriki katika promosheni hiyo kwa uwajibikaji, akibainisha kuwa droo zitaendelea kufanyika kila wiki hadi mwisho wa kampeni.

“Tunawaalika Watanzania wengi kushiriki katika promosheni hii kwa uwajibikaji. Kaulimbiu yetu ni Cheza, shinda boda na ubadilishe maisha yako,” alisema Msonge.




 

Afisa Uwekezaji Mwandamizi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo na Mitaji (UNCDF) , Bw. Abraham Byamungu (wa kwanza kulia) akiwa kwenye picha ya pamoja na Afisa wa Misitu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Bw. Lucas Jacob Sabida wakati wa  warsha ya kujadili sera zinazohusiana na biashara ya kaboni iliyofanyika katika Hoteli ya Slipway jijini Dar es Salaam
Afisa Uwekezaji Mwandamizi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo na Mitaji (UNCDF) , Bw. Abraham Byamungu (kulia) akichangia mada katika warsha ya kujadili sera zinazohusiana na biashara ya kaboni iliyofanyika katika Hoteli ya Slipway jijini Dar es Salaam jana kushoto ni Meneja Mkaazi wa VPenergy Tanzania Bi. Jacqueline Ngulla.
Afisa Uwekezaji Mwandamizi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo na Mitaji (UNCDF) , Bw. Abraham Byamungu (katikati) akiteta jambo na mtaalamu wa biashara ya Carbon Bi. Annika Richter (kushoto) na mtaalamu wa nishati kutoka Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (World Food Program-WFP) Dkt. Geoffrey Ndegwa katika warsha ya kujadili sera zinazohusiana na biashara ya kaboni iliyofanyika katika Hoteli ya Slipway jijini Dar es Salaam.


Na Mwandishi Wetu
SHIRIKA  la Umoja wa Mataifa la Maendeleo na Mitaji (UNCDF), kupitia programu ya nishati safi (Clean Cooking- CookFund” inayofadhiliwa na Umoja wa Ulaya (EU), limeandaa majadiliano ya sera yaliyowakutanisha wadau muhimu wakiwemo Wizara ya Nishati, Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira), Wizara ya Maliasili na Utalii (MNRT), Kituo cha Taifa cha Ufuatiliaji wa Kaboni ( NCMC), wataalamu wa masoko ya kaboni, sekta binafsi pamoja na washirika wa maendeleo, kujadili fursa na changamoto katika kuendeleza biashara ya kaboni nchini Tanzania.

Afisa Uwekezaji Mwandamizi wa UNCDF Bw.Abraham Byamungu, amesema Tanzania ina uwezo mkubwa wa kufanya vizuri katika biashara ya kaboni, sekta inayosaidia kupunguza uzalishaji wa gesi chafu duniani kupitia mbinu mbalimbali ikiwemo miradi ya ufanisi wa matumizi ya nishati, utekelezaji wa Mkakati wa Taifa unaolenga kuwahamasisha asilimia 80 ya Watanzania kutumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034, pamoja na uhifadhi wa misitu.

Akizungumza wakati wa majadiliano yenye mada *“Kuimarisha Ustahimilivu wa Udhibiti na Kuongeza Imani ya Wawekezaji katika Mifumo ya Nishati Safi ya Kupikia Inayotegemea Kaboni,” yaliyofanyika katika Hoteli ya Slipway jijini Dar es Salaam jana, Bw. Byamungu alisema kuwa ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi ni muhimu katika kuweka mazingira bora ya uwekezaji na sera zitakazoiwezesha sekta hiyo kuwanufaisha Watanzania kwa kiwango kikubwa zaidi.

Alieleza kuwa Tanzania ina uwezo mkubwa wa kuvutia wawekezaji katika sekta ya biashara ya kaboni. Hata hivyo, alisema nchi bado ipo nyuma ikilinganishwa na baadhi ya nchi za ukanda huu kama Rwanda, ambayo licha ya kuwa na eneo dogo kijiografia imefanikiwa kupiga hatua kutokana na maandalizi mazuri, mazingira rafiki ya uwekezaji na sera zinazounga mkono ukuaji wa biashara hiyo.

Aidha, alitaja nchi jirani ya Kenya kuwa miongoni mwa nchi zilizopiga hatua kubwa katika biashara ya kaboni kwa kuwashirikisha wadau mbalimbali na kuweka sera zinazowezesha ukuaji wa sekta hiyo.

Hata hivyo, alisisitiza kuwa Tanzania ina nafasi kubwa ya kuzidi nchi nyingi barani Afrika kutokana na ukubwa wa ardhi yake, jitihada zinazoendelea katika matumizi ya nishati safi ya kupikia, pamoja na ukweli kwamba takribani asilimia 34 ya ardhi ya nchi imehifadhiwa kama misitu na maeneo ya wanyamapori, jambo linalotoa fursa kubwa za biashara ya kaboni kupitia upandaji miti na uhifadhi wa misitu.

Katika kuhakikisha biashara ya kaboni inanufaisha nchi, alisema UNCDF inaendelea kuwakutanisha wadau kwa kuandaa majukwaa mbalimbali yanayowaunganisha wataalamu wa sekta hiyo ili kutoa elimu na mwongozo kuhusu namna ya kunufaika na fursa za biashara ya kaboni.

“Lengo letu ni kuwa na majukwaa ya pamoja ambapo tunaweza kujadiliana na kushirikishana uzoefu kutoka nchi nyingine ili tujifunze na kufanya vizuri zaidi,” alisema.

Kwa upande wake, Bw. Lucas Jacob Sabida, Afisa Misitu kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, alisema warsha hiyo ni muhimu kwa kuwa inaleta pamoja wadau mbalimbali kujadili namna biashara ya kaboni inavyoweza kuinufaisha Tanzania kama ilivyofanya katika baadhi ya nchi jirani.

Alisema Serikali, kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais, iko tayari kusaidia ukuaji wa soko la kaboni kupitia Kituo cha Taifa cha Usimamizi wa Biashara ya Kaboni (NCMC) ambacho kimeanzishwa kusaidia kuandaa sheria, miongozo na kanuni mbalimbali ili kuhakikisha nchi inanufaika kikamilifu na biashara hiyo.

Aliongeza kuwa Serikali tayari imeweka mazingira mazuri ya kukuza sekta hiyo kwa kuanzisha NCMC, kituo kinachoratibu masuala yote yanayohusiana na biashara ya kaboni ikiwemo usajili wa miradi, ili kuhakikisha sekta hiyo inakua na kuleta manufaa kwa taifa.

“Tunawapongeza sana UNCDF kwa kuandaa mikutano kama hii ambayo inatupa fursa ya kujadili kwa pamoja namna biashara ya kaboni inaweza kuleta matokeo chanya nchini,” alisema Bw. Sabida.

“Tunao imani kuwa kupitia ushirikiano huu kati ya Serikali na sekta binafsi tutapata mafanikio makubwa katika biashara ya kaboni,” aliongeza.

Pia alieleza kuwa Serikali iko tayari kupitia sera ambazo zinaweza kuwa kikwazo kwa maendeleo ya sekta hiyo kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ili kuweka mazingira bora zaidi kwa ukuaji wa biashara ya kaboni nchini.

Katika kuhitimisha majadiliano hayo, wadau kutoka taasisi mbalimbali za Serikali, sekta binafsi pamoja na washirika wa maendeleo walikubaliana kuimarisha ushirikiano ili kuhakikisha jitihada za pamoja zinatumika kuongeza manufaa ya biashara ya kaboni kwa Tanzania.

Walisisitiza kuwa uratibu mzuri na mshikamano kati ya wadau ni muhimu ili kuhakikisha biashara ya kaboni inachangia ukuaji wa uchumi wa nchi huku ikilinda mazingira kupitia kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia pamoja na usimamizi endelevu wa misitu na ardhi.
Na Mwandishi wetu Dodoma

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amewapongeza wenyeviti na wajumbe wa tume zilizoundwa kutathmini matumizi ya ardhi katika eneo la Ngorongoro Conservation Area kwa kazi kubwa na ya kizalendo waliyoifanya katika kukamilisha majukumu yao.

Rais Samia amesema hayo leo Machi 12, 2026 katika Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma wakati akipokea ripoti za tume hizo, akisema jukumu walilopewa lilikuwa zito kutokana na kuhusisha maoni ya wadau wengi wenye mitazamo tofauti.

Amesema licha ya changamoto hizo, wenyeviti na wajumbe wa tume walitekeleza kazi yao kwa bidii, uadilifu na weledi mkubwa, hali iliyowezesha kukusanywa kwa taarifa muhimu zitakazosaidia kufanya maamuzi sahihi kwa manufaa ya taifa.

Rais Samia amesema baada ya kusikiliza kwa kina taarifa za tume hizo pamoja na kutazama makala ya video iliyoonesha hali halisi ya maeneo yaliyotembelewa, imebainika umuhimu wa kulinda mfumo wa ikolojia unaounganisha maeneo ya Ngorongoro Conservation Area, Pololeti Game Reserve na Lake Natron.

Amesema mfumo huo wa ikolojia ni wa kipekee na una umuhimu mkubwa kwa uhifadhi endelevu wa mazingira pamoja na rasilimali za taifa.

Aidha, Rais Samia amesema taarifa hizo pia zimeonesha uwepo wa rasilimali mbalimbali ikiwemo madini yanayotafutwa duniani ambayo yanapatikana katika maeneo hayo, hivyo kusisitiza umuhimu wa kuyahifadhi kwa manufaa ya taifa na dunia kwa ujumla.

Katika hatua nyingine, Rais Samia amesema taarifa za tume pia zimeonesha changamoto zilizojitokeza katika utekelezaji wa zoezi la uhamaji wa hiari kwa wakazi wa eneo la Ngorongoro kwenda maeneo ya Msomera, Saunyi na maeneo mengine.

Amesema Serikali ilianza zoezi hilo kwa nia njema, lakini imebaini kuwa kulikuwa na mapungufu katika baadhi ya maeneo, hivyo ni muhimu kuyatafakari na kuyarekebisha kabla ya kuendelea na hatua zinazofuata.

Rais Samia amesisitiza kuwa Serikali itaendelea na zoezi hilo la uhamaji wa hiari, lakini kwa kufanya maboresho yatakayozingatia changamoto zilizobainishwa ili kuhakikisha utekelezaji wake unakuwa bora na wenye manufaa kwa wananchi pamoja na taifa.







Top News