Na Munir Shemweta, WANMM

Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeingilia kati mgogoro wa matumizi ya ardhi unaomhusisha mwekezaji Rashid Kwanzibwa, aliyedaiwa kubomoa baadhi ya majengo yaliyokuwa kwenye maeneo ya serikali na kuanzisha miradi bila utaratibu katika eneo la Mamlaka ya Mji Mdogo wa Katoro, Geita.

Akitolea ufafanuzi kuhusu suala hilo leo, tarehe 26 Januari, 2026 jijini Dodoma, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo, amesema wizara yake inaungana na Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kuhakikisha mgogoro unafanyiwa kazi na kukamilika.

Mhe. Dkt Akwilapo amewakumbusha wamiliki wa maeneo yote nchini kuzingatia matumizi yaliyokusudiwa katika hati miliki zao, na endapo mmiliki ana mpango wa kuendeleza eneo lake kwa matumizi tofauti na yaliyotolewa katika hati, ni lazima apate kibali cha mabadiliko ya matumizi kama sheria inavyoelekeza.

''Hatua hiyo itahakikisha maeneo yanaendelezwa kwa kuzingatia mpango, na hivyo kuondoa migongano ya matumizi, kutunza mazingira, na kuweka nadhifu miji yetu''. Amesema

Kwa mujibu wa Dkt. Akwilapo, uendelezaji wowote unaofanyika sharti uzingatie sheria za uendelezaji miji, ikiwa ni pamoja na kupata vibali vyote vinavyotolewa na mamlaka zote za serikali. Kwa sasa, wataalamu wa Wizara wameungana na TAMISEMI kushughulikia suala hilo, na baada ya uchunguzi kukamilika, kutatolewa taarifa rasmi ya pamoja.

Uamuzi wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuingilia kati sakata hilo unafuatia kusambaa kwa picha mjengeo katika mitandao mbalimbali ya kijamii, ikionesha Kamati ya Fedha na Uchumi ya Halmashauri ya Wilaya ya Geita ikilazimika kusimamisha shughuli za mradi wa ujenzi wa vibanda vya maduka kwenye eneo la viwanja vya CCM Katoro, huku ikidaiwa mwekezaji kuingia mipaka ya serikali ya kijiji katika Kitongoji cha Katoro Center kilichopo mji mdogo wa Katoro mkoani Geita.


DAR ES SALAAM, 26 Januari 2026. Africa Pension Fund Limited (APeF) leo imezindua rasmi Mfuko wa Ziada, ambao ni mfuko wa kwanza wa uwekezaji wa pamoja katika soko la fedha nchini Tanzania unaojumuisha mafao ya bima ya maisha, hatua inayoweka alama muhimu katika kupanua upatikanaji wa suluhisho za uwekezaji zilizo chini ya udhibiti. 

Hafla ya uzinduzi imefanyika katika Hoteli ya KingJada, Morocco Square, jijini Dar es Salaam. Kipindi cha awali cha uuzaji wa vipande kupitia mfuko huu kinaanza leo tarehe 26 Januari hadi 25 Februari 2026.

Hafla ya uzinduzi huo ilihudhuriwa na mgeni rasmi, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), CPA Nicodemus Mkama, ikihudhuriwa pia na wawakilishi kutoka Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), mifuko ya hifadhi ya jamii, wasimamizi wa mifuko, madalali, taasisi za kibenki na bima, pamoja na wanahabari.

Mfuko wa Ziada umebuniwa kuwasaidia wawekezaji kuweka akiba na kukuza fedha zao kupitia uwekezaji wenye nidhamu katika soko la fedha, ukiwa na faida ya ziada ya ulinzi wa bima ya maisha kwa wawekezaji binafsi wanaokidhi vigezo. 

Mfuko huu umerahisishwa kiutendaji, kwa kuwawezesha wawekezaji kuanza kwa urahisi, kuongeza uwekezaji wakati wowote, na kupata fedha zao ndani ya siku tatu za kazi.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Ofisa Mtendaji Mkuu wa APeF, Bw. Mfaume Kimario, alisema, Ziada imeundwa kwa wawekezaji wanaotaka njia rahisi na za kuaminika za kukuza fedha zao bila kupoteza uwezo wa kupata fedha zao pindi zinapohitajika. 

Huu ni mfuko imara katika soko la fedha unaopatikana kwa urahisi, wenye ulinzi wa bima ya maisha kwa wawekezaji wanaokidhi vigezo ukianzia na thamani halisi ya uwekezaji (vipande), ya chini kabisa ya shilingi 250,000.

Bima hiyo hutoa kinga sawa na asilimia 50 ya thamani halisi ya uwekezaji (vipande) hadi kiwango cha juu cha thamani kilichohakikishwa cha shilingi milioni 100, na kiwango cha juu cha malipo ya bima cha shilingi milioni 50.

Akizungumza kwa niaba ya Mwenyekiti na Bodi ya Wakurugenzi, Dkt. Hamisi Kibola, Mjumbe wa Bodi ya APeF, aliipongeza CMSA kwa hatua zilizofikiwa katika kuendeleza masoko ya mitaji nchini Tanzania na kwa kukuza ukuaji na uhai unaoonekana sokoni kwa sasa.

 Alibainisha kuwa kiwango cha uwekaji akiba nchini Tanzania bado kiko chini ya asilimia 3, na akatoa wito wa kuimarishwa kwa ushirikiano kati ya wasimamizi na wadau wa sekta ya fedha ili kujenga utamaduni imara wa kujiwekea akiba unaojengwa juu ya taaluma, uaminifu, elimu ya fedha na upatikanaji rahisi wa huduma. 

Aliongeza kuwa ndiyo sababu APeF ilianzishwa, ubunifu ukiwa kama msingi wake, ili kuongeza wigo kwa vitendo njia za uwekaji akiba na uwekezaji kupitia mifuko ya uwekezaji wa pamoja, mipango binafsi ya pensheni inayounganisha suluhisho za bima na masoko ya mitaji.

Mfuko wa Ziada umeandaliwa kwa ushirikiano na taasisi washirika muhimu, ambapo Alliance Life Assurance Limited ni mtoa bima, Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) ni Mtunza Dhamana na Mdhamini. Wawekezaji wanaweza kupata huduma za Mfuko wa Ziada kupitia benki wakusanyaji zikiwemo CRDB Bank, NMB Bank, Exim Bank, Azania Bank, COOP Bank, NBC na Mwanga Hakika Bank, pamoja na kupitia mawakala walioidhinishwa na DSE na majukwaa ya kidijitali ya APeF.

“Tunaalika Watanzania kufanya suala la kuweka akiba kuwa utamaduni wao kupitia Ziada. Unapoweka akiba kwa uthabiti, unaimarisha familia yako, kuinua jamii yako, na kuunga mkono maendeleo ya taifa. Ziada inakupa mahali rahisi pa kuanzia, kukua hatua kwa hatua, na kulinda kile kilicho muhimu zaidi,” aliongeza Ofisa Mtendaji Mkuu wa APef, Bw. Kimario.

Kwa upande wake Ofisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), CPA. Nicodemus Mkama alisema kuidhinishwa kwa mfuko wa ziada kunaendelea kuleta chachu zaidi katika maendeleo ya uwekezaji kwenye mifuko hiyo na kuifanya idadi ya mifuko hiyo ya uwekezaji wa pamoja kufikia 26.
Ofisa 
Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana, (CMSA), CPA Nicodemus Mkama, akikabidhi waraka wa ofa kwa Kaimu Mwenyekiti wa Bodi ya Africa Pension Fund (APeF), Dkt. Hamisi Kibola (wa tatu kushoto), kuashiria uzinduzi rasmi wa Mfuko wa Uwekezaji wa Pamoja wa Ziada Fund, jijini Dar es Salaam leo. Wa pili kushoto ni Ofisa Mtendaji Mkuu wa APeF, Bw. Mfaume Kimario, pamoja na wadau wengine wa Mfuko wa Ziada; kuanzia kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa Alliance Life, Bw. Byford Mutikwasa, Bi. Tupokigwe Mwalwisi kutoka NBC na Bw. Lusungu.Ofisa Mtendaji Mkuu wa Africa Pension Fund (APeF), Bw. Mfaume Kimario, akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi rasmi wa Mfuko wa Uwekezaji wa Pamoja wa Ziada Fund, jijini Dar es Salaam leo.

Kaimu Mwenyekiti wa Bodi ya Africa Pension Fund (APeF), Dkt. Hamisi Kibola akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi rasmi wa Mfuko wa Uwekezaji wa Pamoja wa Ziada Fund, jijini Dar es Salaam leo.

Baadhi ya wadau wakihudhuria hafla ya uzinduzi rasmi wa Mfuko wa Uwekezaji wa Pamoja wa Ziada Fund unaoendeshwa na Africa Pension Fund (APeF).

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Africa Pension Fund (APeF), Bw. Mfaume Kimario (kushoto) akizungumza na baadhi ya wadau wa Mfuko wa Uwekezaji wa Pamoja wa Ziada Fund wakati wa hafla ya uzinduzi wa mfuko huo, jijini Dar es Salaam leo.

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana, (CMSA), CPA Nicodemus Mkama (katikati) , Kaimu Mwenyekiti wa Bodi ya Africa Pension Fund (APeF), Dkt. Hamisi Kibola ( wa nne kushoto) na Ofisa Mtendaji Mkuu wa APeF, Bw. Mfaume Kimario ( wa nne kulia ) wakipiga picha ya pamoja na baadhi ya wafanyakazi wa taasisi hiyo baada uzinduzi rasmi wa Mfuko wa Uwekezaji wa Pamoja wa Ziada Fund, jijini Dar es Salaam leo.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuweka kipaumbele kikubwa katika uendeshaji wa uchumi, utoaji wa huduma za Taasisi za Umma pamoja na ukusanyaji wa mapato kwa kutumia mifumo ya kidigitali.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo tarehe 26 Januari 2026 alipokutana na Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Angellah Kairuki, pamoja na watendaji wakuu wa Wizara hiyo, Ikulu Zanzibar.

Amesisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya Wizara za Muungano na Zanzibar, ikiwemo kuharakisha ujenzi wa Kituo cha Ukusanyaji wa Taarifa (Data Centre) Zanzibar, kuboresha miundombinu ya mawasiliano na kuongeza upatikanaji wa intaneti ya kasi.

Kwa upande wake, Waziri Angellah Kairuki amemhakikishia Rais Dkt. Mwinyi kuwa Wizara yake itaendelea kushirikiana kwa karibu na Zanzibar ili kuhakikisha upatikanaji wa huduma za mawasiliano zilizo salama, za uhakika na zenye viwango vya kitaifa na kimataifa.





Mhe. Balozi Dkt. Batilda Burian, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, ameipongeza Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) kwa mchango wake mkubwa katika kuchagiza mageuzi ya sekta ya kilimo kutoka kilimo cha kujikimu kwenda kilimo cha kibiashara.

Mhe. Mkuu wa Mkoa ametoa pongezi hizo alipotembelea banda la TADB katika Maadhimisho ya Wiki ya Huduma za Fedha Kitaifa yaliyofanyika katika Viwanja vya Usagara, jijini Tanga.

Katika banda la TADB, Mhe. Mkuu wa Mkoa alipokelewa na wafanyakazi wa benki hiyo na kupatiwa muhtasari wa maendeleo na ukuaji wa benki, pamoja na huduma mbalimbali zinazotolewa katika minyororo ya thamani ya kilimo, mifugo na uvuvi, hususan katika Mkoa wa Tanga na Kanda ya Kaskazini kwa ujumla.

Aidha, TADB inaishukuru Wizara ya Fedha pamoja na Kamati ya Maandalizi ya maadhimisho hayo kwa kutambua mchango wa benki katika kutoa huduma bora za kifedha kupitia mabanda na utoaji wa elimu ya fedha kwa wananchi wa Mkoa wa Tanga na mikoa ya jirani.
 
Kutokana na mchango huo, TADB ilitambuliwa kama mshindi wa nafasi ya tatu miongoni mwa mabenki na taasisi za fedha, na kukabidhiwa tuzo maalum.

Maadhimisho ya Wiki ya Huduma za Fedha Kitaifa yamehitimishwa leo tarehe 26 Januari 2026 katika Viwanja vya Usagara, jijini Tanga.



Na Mwandishi Wetu

WANAFUNZI wa Chuo cha Kodi (ITA) wameadhimisha Siku ya Kimataifa ya Forodha kwa mjadala wa kitaaluma kuhusu jukumu la utendaji wa Himaya Moja ya Forodha (SCT) na Vituo vya Pamoja vya Forodha Mpakani (OSBP) katika kulinda jamii.

Akifungua maadhimisho hayo ambayo yamefanyika kwa mara ya kwanza Chuoni, Mkuu wa Chuo cha Kodi Prof. Isaya Jairo amesema ITA inafanya shughuli za forodha kwa kutoa mafunzo kwa watumishi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na wadau wake ya namna ya kukusanya mapato yatokanayo na forodha hivyo siku hii ni muhimu kwa ITA.

“Forodha pamoja na kukusanya kodi pia inalinda jamii kwa kuhakikisha kila bidhaa inayopita katika mipaka kuingia ndani ya nchi ni salama,” alisema Prof. Jairo na kuongeza kwamba Siku ya Kimataifa ya Forodha ni tukio muhimu kwani jukumu kubwa la forodha pia ni kulinda mipaka ya nchi.

Amesema kuwa Forodha ni eneo muhimu kwa Mamaka ya Mapato Tanzania kwani linakusanya asilimia 40 ya makusanyo ya TRA.

Katika hatua nyingine, Prof. Jairo amewataka wanafunzi wa ITA kuanzisha klabu ya Forodha ili kuendeleza taaluma ya Forodha kwani Chuo kinajitahidi kufundisha uhalisia wa masuala ya forodha hivyo ni jukumu la wanafunzi kuonyesha kwamba wamebobea.

Katika Mjadala wa kitaaluma wanafunzi wa Chuo cha Kodi wameelezwa tofauti kati ya Himaya Moja ya Forodha na Vituo vya pamoja Mpakani na kwa ujumla jinsi forodha inavyotumika kudhibiti bidhaa zinazoingia nchini lengo likiwa ni kuhakikisha jamii inakuwa salama.

Msingi wa mjadala huo ni kauli mbiu ya Siku ya Kimataifa ya Forodha, isemayo,”Forodha Inalinda Jamii kwa Umakini na Kujitoa”.

Watoa mada katika mjadala huo walikuwa ni watumishi wa TRA ndugu Mbogo Kerenge na Ndugu Leonard Mutiba, mjadala ambao uliwapa fursa wanafunzi kuuliza maswali na kupata majibu ikiwa ni sehemu ya kuwapa uelewa zaidi wa shughuli za forodha.

Pamoja na Mkuu wa Chuo cha Kodi, maadhimisho hayo pia yalihudhuriwa na Naibu Mkuu wa Chuo cha Kodi Utawala, Mipango na Fedha Ndugu Emmanuel Masalu, Dk. Cyril Chimilia kwa Niaba ya Naibu Mkuu wa Chuo cha Kodi Taaluma, Utafiti na Ushauri Elekezi, Ndugu Mary Ruhara kwa niaba ya Mkuu wa Idara ya Mafunzo ya Forodha Chuo cha Kodi pamoja na Rais wa Serikali ya Wanafunzi wa ITA (ITASO), Ndugu Karimu Kitundu.

Wahadhiri wa masomo ya Forodha, wafanyakazi wengine wa Chuo pamoja na wanafunzi wa Chuo pia wameshirii wa mjadala huo.

Siku ya Forodha huadhimishwa kila Mwaka tarehe 26 Januari kwa kufanya shughuli mbalimbali ambapo ITA ikiwa ni mdau wa Forodha na Mwanachama wa Mtandao wa Kimataifa wa Vyuo vya Forodha (INCU) Vyuo Vikuu vya Forodha imeadhimisha kwa kajadiliana namna SCT na OSBP zinavyotumika katika Forodha.


Afisa Forodha Mkuu Lenard mutiba akifafanua jambo mbele ya wanafunzi wa chuo cha kodi jijini Dar es salaam jana, wameadhimisha Siku ya Kimataifa ya Forodha kwa mjadala wa kitaaluma kuhusu jukumu la  utendaji wa Himaya Moja ya Forodha (SCT) na Vituo vya Pamoja vya Forodha Mpakani (OSBP)  katika kulinda jamii.



London, Uingereza .

Katika mwendelezo wa ziara yake Nchini Uingereza, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Mhe, prof. Kitila Mkumbo, amekutana na kufanya mazungumzo na Uongozi wa Mfuko wa Kimataifa wa Uwekezaji Sino American Global Fund (SinoAm LLC).

Mazungumzo ya Mheshimiwa Waziri na uongozi wa Mfuko huo yalihusisha utayari wa SinoAm LLC kuwekeza kiasi kinachoweza kufikia dola za Marekani bilioni 5 nchini Tanzania.

Uwekezaji huo, unatarajiwa kufanyika kupitia miradi ya Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP) na utazingatia vipaumbele vya maendeleo ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan na utatekezwa kwa awamu mbalimbali.

Waziri Mkumbo aliipongeza SinoAm LLC kwa kuonesha dhamira ya dhati ya kuwekeza kiasi kikubwa cha mitaji nchini Tanzania, akibainisha kuwa Serikali imeendelea kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji ili kuvutia wawekezaji wakubwa wa kimataifa.

“Tanzania ina utulivu wa kisiasa, sera rafiki za uwekezaji, na dira ya muda mrefu ya maendeleo inayotoa uhakika na ulinzi kwa uwekezaji wa kimkakati” Alisema Prof. Mkumbo.

Kwa upande wake Bw. Najib Choufani, Mwenyekiti wa Mfuko huo, alibainisha kuwa SinoAm LLC imefanya tathmini ya kina ya mazingira ya uwekezaji nchini Tanzania na kubaini fursa zenye tija kubwa, ikiwemo ujenzi na uendeshaji wa barabara za kisasa za kulipia (toll expressways).

Aidha, miradi ya reli ya kiwango cha kimataifa (SGR), pamoja na miundombinu muhimu ya uchukuzi na nishati inayochochea ukuaji wa uchumi na kuongeza ushindani wa Tanzania kikanda ni miongo mwa maeneo yanayolengwa.

Katika mkutano huo, Mhe. Waziri ameambatana na Katibu Mkuu Dkt. Tausi M. Kida, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo maalumu ya Kiuchumi TISEZA Bw. Giread Teri, huku uongozi wa SinoAm LLC pia uliambatana na Bw. Tarek Choufani, Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko huo, ambaye alieleza kuwa SinoAm ina uzoefu mpana wa kimataifa katika kusimamia miradi mikubwa ya miundombinu na iko tayari kuleta si tu mitaji mikubwa, bali pia utaalamu wa kiufundi, mifumo ya kisasa ya usimamizi na mbinu bora za kimataifa nchini Tanzania.




Na Mwandishi wetu

SHIRIKA la INADES-Formation Tanzania limezindua kitalu cha miti chenye lengo la kuzalisha miche 500,000 ifikapo mwaka 2027, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kukabiliana na changamoto za uharibifu wa mazingira na mabadiliko ya tabianchi.

Kitalu hicho, ambacho pia kitazalisha miche ya matunda pamoja na miche ya miti ya asili, kitahudumia Wilaya za Bahi, Kondoa na Chemba, hususan katika vijiji vya mradi wa shirika hilo pamoja na vijiji jirani.

Akizindua mpango huo, Mkurugenzi wa Shirika la INADES-Formation Tanzania, Jacqueline Nicodemus, alisema uanzishwaji wa kitalu hicho utasaidia kuongeza kasi ya kampeni za upandaji miti katika wilaya hizo tatu na kukabiliana na changamoto za muda mrefu za upatikanaji wa miche bora.

Alisema kitalu hicho, ambacho kinaanzishwa kwenye Kituo cha Mafunzo ya Kilimo Mseto katika Maeneo yenye ukame (DATC), kitatumika pia kama kituo cha kuhifadhi miche, kufanya tafiti za miti na kutekeleza shughuli nyingine zinazohusiana na kilimo mseto. Hatua hiyo itaongeza mchango wa shirika katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na kuimarisha uhifadhi wa mazingira.

“Shirika limesukumwa kuanzisha kitalu hiki kutokana na changamoto kubwa ya uharibifu wa mazingira, upungufu wa miti na athari za mabadiliko ya tabianchi zinazozikumba wilaya za Kondoa, Chemba na Bahi,” alisema Nicodemus.

Aliongeza kuwa maeneo hayo ni ya ukame na yamekuwa yakikumbwa na ukataji miti hovyo, uhaba wa miche bora na kupungua kwa rutuba ya ardhi, hivyo uanzishwaji wa kitalu hicho utahakikisha upatikanaji wa miche bora, hususan ya asili, itakayosaidia kurejesha mazingira na kuboresha uzalishaji wa kilimo.

Aidha, alisema upandaji wa miti ya matunda utaongeza kipato cha kaya na kuimarisha ustahimilivu wa jamii dhidi ya athari za mabadiliko ya tabianchi.

Amesema shurika hilo limeweka mikakati na miundombinu madhubuti ya uzalishaji wa miche, pamoja na kuwajengea uwezo wakulima, vikundi vya jamii na maafisa ugani kuhusu uzalishaji na utunzaji wa miche ili kuhakikisha lengo la kuzalisha miche 500,000 linafikiwa ifikapo mwaka 2027.

Nicodemus alisema shirika litashirikiana na serikali za vijiji vya mradi, wadau wa mazingira na taasisi za utafiti, pamoja na kutumia teknolojia na mbinu rafiki za kilimo hifadhi, ili kuhakikisha upatikanaji endelevu wa maji na miche katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Ameongeza kuwa mkazo utawekwa zaidi kwenye uzalishaji wa miti ya asili kwa kuwa ina uwezo mkubwa wa kustahimili mazingira ya ukame, kurejesha mifumo ya ikolojia na kuhifadhi bioanuai. Miti hiyo pia husaidia kulinda vyanzo vya maji na kuboresha rutuba ya ardhi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Mafunzo wa Shirika hilo, Bwana Michael Kihwele, alisema upandaji wa miti ya matunda unalenga kuboresha lishe ya kaya na kuongeza kipato huku ukiendelea kuchangia uhifadhi wa mazingira.

Akizungumzia ushirikishwaji wa jamii katika vijiji vya mradi, alisema shirika litatoa mafunzo ya vitendo kuhusu uzalishaji, upandaji na utunzaji wa miche, pamoja na kuunda na kuimarisha vikundi vya mazingira na vitalu vidogo vya miche katika ngazi ya vijiji.

Alisema pia shirika litahamasisha ushiriki wa jamii katika upandaji na ufuatiliaji wa miti iliyopandwa, na kuwawezesha vijana na wanawake kushiriki kama wazalishaji na wasambazaji wa miche.

Hatua hiyo itasaidia jamii kumiliki mradi, kuongeza uelewa wa masuala ya mazingira na kuchukua hatua za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Kitalu hicho kinatarajiwa kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi kwa kusaidia kurejesha uoto wa asili, kupunguza mmomonyoko wa udongo, kuhifadhi maji na kuongeza ustahimilivu wa jamii dhidi ya ukame na majanga ya tabianchi.

Shirika hilo limeendelea kuhimiza wadau kushirikiana na kuunga mkono jitihada hizo kwa kuchukua hatua za vitendo katika kulinda mazingira kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

INADES-Formation Tanzania ni shirika lisilo la kiserikali (NGO) lililoanzishwa mwaka 1989, likiwa ni sehemu ya mtandao wa kimataifa wa INADES-Formation, lenye lengo la kuboresha maisha na ustawi wa jamii za vijijini, hususan wakulima wadogo na wafugaji.
Mkurugenzi wa shirika la INADES-Formation Tanzani, Jacqueline Nicodemus akipokea cheti cha ushindi kwenye maonesho ya Kilimo Misitu wakati wa Kongamano la Kumi la  maonesho hayo yaliyofanyika  Musoma, Mkoani Mara hivi karibuni

Mkurugenzi wa shirika la INADES-Formation Tanzani,  Jacqueline Nicodemus akionyesha cheti cha ushindi wakati wa Kongamano la  Kumi wakati wa maonesho ya Kilimomisitu yaliyofanyika Musoma, Mara hivi karibuni.

Mkurugenzi wa shirika la INADES-Formation Tanzania,  Jacqueline Nicodemus  akishiriki katika kampeni ya upandaji miti wakati wa Kongamano la kumi la Kilimo Misitu lililofanyika Musoma mkoani Mara hivi karibuni. Kongamano hilo lilivutia zaidi ya washiriki 6,000 na kuona miti 860 ikipandwa ambapo wanafunzi wa shule za msingi wilayani humo walishiriki pia
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

CHUO Kikuu Cha Dar es Salaam (UDSM), kupitia Shule Kuu ya Madini na Jiosayansi, kimepokea msaada wa kompyuta 10 kutoka Kampuni ya AngloGold Ashanti kwa ajili ya kuimarisha shughuli za ufundishaji na utafiti, ikiwa ni muendelezo wa ushirikiano kati ya taasisi hizo mbili.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Januari 26, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya makabidhiano, Makamu Mkuu wa Chuo, Profesa William Anangisye, amesema vifaa hivyo vitasaidia kuongeza ufanisi katika mchakato wa kujifunza, kufundishia na kufanya tafiti kwa wanataaluma na wanafunzi.

Amesema kupitia msaada huo, chuo kinatarajia kuendelea kuboresha mazingira ya elimu ya juu na kuchangia maendeleo ya taifa kwa ujumla.

Aidha, Prof. Anangisye amezitaka taasisi na kampuni nyingine zinazojihusisha na sekta ya madini kujitokeza kutoa mchango wao kwa chuo hicho ili kusaidia kukijengea uwezo zaidi wa kutekeleza majukumu yake.

“Msaada wowote utakaotolewa utakuwa na mchango mkubwa katika kukisaidia chuo kufikia malengo yake ya kulielimisha taifa kwa manufaa ya maendeleo ya nchi,” amesema Prof. Anangisye.

Kwa upande wake, Makamu wa Rais wa Kampuni ya AngloGold Ashanti Kanda ya Afrika, Bw. Simon Shayo, amesema kukabidhi kompyuta hizo ni sehemu ya mkakati wa kampuni hiyo kuhakikisha UDSM inakuwa na teknolojia inayokwenda sambamba na mahitaji ya sasa ya elimu na sekta ya madini.

Amesema uwepo wa kompyuta za kisasa chuoni hapo utasaidia kuwaandaa wanafunzi vizuri zaidi, ambao baadaye ni rasilimali muhimu kwa sekta ya madini na maendeleo ya nchi.

“Tunajenga wigo mpana wa ushirikiano kati yetu na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam katika maeneo ya ufundishaji, utafiti na ushauri wa kitaalamu,” amesema Bw. Shayo.

Ameongeza kuwa AngloGold Ashanti itaendelea kushirikiana na UDSM, ikiamini kuwa sekta binafsi ina jukumu la msingi katika kusaidia maandalizi ya wahitimu ili kukidhi mahitaji ya soko la ajira na maendeleo ya taifa.










MAMLAKA ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) imezindua Mfuko wa Uwekezaji wa Pamoja wa Kampuni ya Africa Pension Fund Limited (APEF) unaoitwa Ziada Fund.

Akizungumza leo Januari 26,2026 jijini Dar es Salaam,Ofisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka hiyo CPA Nicodemus Mkama, amesema uzinduzi wa Mfuko huo ni baada ya idhini iliyotolewa na mamlaka hiyo baada ya Africa Pension Fund Limited kukidhi matakwa ya Sheria.

Hata hivyo amesema uzinduzi wa mfuko huo ni tukio la kihistoria ambalo lina mchango mkubwa katika maendeleo na ustawi wa masoko ya mitaji na uchumi kwa ujumla hapa nchini.

“Ziada Fund ni mfuko wa uwekezaji wa pamoja wenye ubunifu wa kuwekeza katika Masoko ya Mitaji na Masoko ya Fedha; na ambao Unatoa Bima ya Maisha kwa wawekezaji.”

Aidha amesema sekta ya masoko ya mitaji hapa nchini ina wadau wengi wanaounga mkono utekelezaji wa mikakati ya maendeleo ya masoko ya mitaji inayoakisiwa kwa uanzishaji wa bidhaa mpya na bunifu, zinazotoa wigo mpana kwa wawekezaji wa ndani na wa kimataifa kushiriki katika masoko ya mitaji hapa nchini.

“Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) ina jukumu la kuendeleza na kusimamia masoko ya mitaji hapa nchini, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kwamba shughuli katika masoko ya mitaji zinafanyika kwa kufuata sheria, taratibu na miongozo ili kuleta uwazi na haki kwa washiriki wote.

“Pamoja na jukumu la kusimamia na kuendeleza masoko ya mitaji hapa nchini, CMSA pia ina jukumu la kuidhinisha maombi ya kuanzisha bidhaa mpya katika masoko ya mitaji, ikiwa ni pamoja na Mifuko ya Uwekezaji wa Pamoja.”



Na Mwandishi Wetu


MAMLAKA ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) imesema katika kipindi cha miaka mitano, kumekuwa na maendeleo makubwa na ustawi mzuri wa uwekezaji katika mifuko ya uwekezaji wa pamoja.

Imefafanua katika kipindi kilichoishia Disemba 2025 imeongezeka kwa asilimia 65.10 na kufikia Sh. trilioni 4.35, ikilinganishwa na Sh. trilioni 2.64 katika kipindi kilichoishia Disemba mwaka 2024 huku ikisisitiza Katika kipindi cha miaka mitano, kumekuwa na maendeleo na ustawi mzuri katika mifuko ya uwekezaji wa pamoja, ambapo mifuko mipya na bunifu imeanzishwa.


Hayo yameelezwa leo Januari 26,2026 jijini Dar es Salaam na Ofisa Mtendaji wa Mamlaka ya Mitaji na Dhamana (CMSA), CPA. Nicodemus Mkama katika hafla ya uzinduzi wa Mfuko wa Uwekezaji wa Pamoja wa Kampuni ya Africa Pension Fund Limited (APEF) unaoitwa Ziada Fund.

“Mifuko hii inatoa fursa kuwekeza kwa kiwango cha chini na hivyo kuvutia wawekezaji wa kada mbalimbali ikiwa ni pamoja na vijana, wanawake na makundi maalumu, kuwekeza katika masoko ya mitaji.

“Hatua hii imewezesha kuongezeka kwa thamani ya uwekezaji katika mifuko ya uwekezaji wa pamoja kwa asilimia 520.41 na kufikia Sh. trilioni 4.4 Disemba 2025, ikilinganishwa na Sh. bilioni 701.46 Disemba 2021.

“Kuidhinishwa kwa Mfuko wa Ziada kunafanya Mifuko ya Uwekezaji wa Pamoja hapa nchini kufikia 26, hivyo, tunatarajia mfuko huu kuchochea zaidi maendeleo na ustawi wa uchumi wanchi yetu. “

Kuhusu Mfuko wa Ziada amesema una malengo mahsusi ya kuwekeza katika masoko ya mitaji, ikiwa ni pamoja na kuwekeza katika Hatifungani za Serikali, Hatifungani za Kampuni, Dhamana za Serikali za muda mfupi na Amana katika benki za biashara.

Aidha, amesema Mfuko huo unatoa Bima ya Maisha (Life Insurance) kwa wawekezaji inayofikia asilimia 50 ya Thamani ya Uwekezaji, hivyo kuwafanya wawekezaji kufaidika na uwekezaji katika masoko ya mitaji; na kupata manufaa ya bima ya maisha.

“Bima ya maisha ni nguzo muhimu ya usalama wa kifedha kwa wananchi, kwani husaidia kulinda familia dhidi ya athari za kifedha zinazoweza kujitokeza endapo muwekezaji atafariki, kupata ulemavu wa kudumu, au kukumbwa na majanga yasiyotarajiwa.

“Kupitia bima ya maisha, familia huweza kuendelea na maisha kwa uthabiti, ikiwa ni pamoja na kuweza kugharamia mahitaji ya msingi kama elimu ya watoto, huduma za afya, na marejesho ya mikopo, hivyo kupunguza utegemezi wa kifedha kwa ndugu au jamii,”amesema CPA.Mkama

Akifafanua zaidi amesema Bima ya Maisha huchangia kukuza utamaduni wa kupanga na kujiandaa kwa siku zijazo, jambo linaloimarisha ustawi wa kaya na uchumi wa taifa kwa ujumla.

Hivyo amesisitiza kuanzishwa kwa Mfuko wa Ziada ni hatua muhimu katika utekelezaji wa Mpango Mkuu wa Maendeleo ya Sekta ya Fedha 2020/21 – 2029/30 ambao pamoja na mambo mengine, una lengo la kuwezesha masoko ya mitaji kuwa na bidhaa bunifu zinazokidhi mahitaji ya wawekezaji, na hivyo kuchochea uchumi shindani, himilivu na jumuishi kwa maendeleo endelevu kwa watanzania wote.

Amesema ili kufikia malengo ya Mpango Mkuu wa Sekta ya Fedha, ni muhimu kwa wananchi kutumia fursa za uwekezaji zinazojitokeza, ikiwa ni pamoja na kuwekeza katika mifuko ya uwekezaji wa pamoja. Kuanzishwa kwa Mfuko wa Ziada ni mojawapo ya fursa za kufanikisha azma hii.

“Mfuko huu unatoa fursa kwa wawekezaji wa ndani na kimataifa kushiriki na kuwezesha upatikanaji wa maendeleo endelevu kwa watanzania wote. Hivyo nawapongeza Bodi na Menejimenti ya Africa Pension Fund Limited kwa kuja na ubunifu huu.

“Pia Mfuko wa Ziada unaendeshwa na kampuni ya Africa Pension Fund Limited ambaye ni Meneja wa Mfuko na Benki ya NBC (NBC Bank Limited) ambaye ni Mtunza Dhamana wa Mfuko (Custodian).

“Aidha, Kampuni ya Alliance Life Insurance ndiyo kampuni inayotoa Bima ya Maisha (Life Insurance) kwa wawekezaji wa Mfuko huu. Nazipongeza sana Kampuni hizi kwa kuja na ubunifu wa kuanzisha Mfuko huu wenye manufaa makubwa kwa wananchi.”

Hata hivyo amesema uwekezaji katika Mfuko wa Ziada una manufaa katika ustawi wa jamii na maendeleo ya uchumi hapa nchini ikiwemo kuchangia katika utekelezaji wa Sera ya Taifa ya uwezeshaji wananchi kiuchumi kwa kuwezesha makundi mbalimbali ya jamii.

“Ikiwa ni pamoja na watu wa kipato cha chini kuwekeza kwa pamoja katika dhamana za masoko ya mitaji.Pia wawekezaji watapata faida ya ongezeko la thamani katika uwekezaji wao (Net Asset Value), ikiwa uwekezaji utafanyika kwa mujibu wa Sera ya Uwekezaji kwa lengo la kuongeza ufanisi na kupata faida.

“Aidha mfuko huu unatoa anuwai ya uwekezaji kwa wananchi ambapo wawekezaji watapata fursa ya fedha zao kuwekezwa katika maeneo mbalimbali na hivyo kupunguza vihatarishi. “






Top News