Afisa Uhusiano na Huduma kwa Wateja TANESCO Mkoa wa Ruvuma Alan Njiro, amesema kuwa umeme ni nishati muhimu lakini ni hatari endapo hautatumika kwa usahihi, kwani unaweza kusababisha madhara makubwa kwa jamii.

Njiro ameyasema hayo Januari 27 alipotembelea shule ya msingi Mwenge na Shule ya sekondari Nasuri iliyopo Wilayani Namtumbo mkoani Ruvuma wakati wa mwendelezo wa ziara yake ya utoaji wa elimu ya matumizi salama ya umeme kwa wananchi na wanafunzi wa shule za msingi na sekondari,  kuhusu faida na athari za umeme.

Kwa mujibu wa Njiro, elimu hiyo inalenga kuwajengea wanafunzi uelewa mapema ili waweze kujilinda dhidi ya hatari za umeme na pia kuifikisha elimu hiyo kwa familia na jamii zao.

Ameeleza kuwa transfoma hutumika kupoza umeme kabla ya kusambazwa majumbani, hivyo ni hatari kwa mtu yeyote kuichezea au kukaribia miundombinu hiyo.

Njiro amewataka watoto kutoa taarifa kwa wazazi au walezi wao pindi wanapoona mtu akichezea transfoma au nyaya za umeme, ili hatua za haraka zichukuliwe, ameongeza kuwa ushirikiano kati ya TANESCO na jamii ni muhimu katika kuzuia ajali zinazoweza kujitokeza.

TANESCO Ruvuma imeendelea kutoa elimu kwa wananchi kama sehemu ya mkakati wa kupunguza madhara yatokanayo na umeme, na kulinda miundombinu kwa kuzingatia  majukumu yake muhimu ya kuzalisha, kusafirisha, kusambaza na kuuza umeme nchini.






 

Na. Janeth Raphael MichuziTv - Dodoma 

‎Naibu waziri wa Viwanda na Biashara Dennis Londo, amesema kuwa ujio mpya wa stakabadhi za ghala unawakumbusha wakulima changamoto walizopitia kupitia vyama vyao vya ushirika. Aidha, amebainisha kuwa kazi kubwa iliyopo sasa ni kuimarisha imani ya wananchi kwa serikali na taasisi zake, ikiwemo mfumo huu wa stakabadhi za ghala.

Londo ‎ameyazungumza  hayo wakati WRRB Uzinduzi wa Mfumo na kuazimisha Miaka 20 ya Kuimarisha Biashara ya Kilimo Tanzania Kupitia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala 27, 2026, Jijini Dodoma.

‎Amesema, "Ujio mpya wa stakabadhi ghalani na yenyewe pia inawakumbusha changamoto wakulima hawa kule walikotokea kupitia vyama vyao vya ushirika. Kazi kubwa ambayo nayo sasa hivi ni imani ya wananchi kwa serikali. Imani ya wakulima kwa taasisi za Serikali na mifumo ya Serikali ikiwemo hii ya stakabadhi za ghala." amesema waziri Londo

‎AmeelezaAmeeleza kuwa, "Wakulima wanapovuna na kupeleka mazao ghalani, wanategemea malipo mara moja kwa sababu changamoto zao ni kusuluhisha madeni, mikopo, ada za watoto, na huduma za afya. Hata hivyo, wakulima hawa wanaona kama wanakopesha mazao yao kutokana na kucheleweshwa malipo, hali inayotokana na ukosefu wa imani."

‎Amesema zaidi kuwa, "Kazi kubwa ambayo mnafanya ni jema katika kumkomboa Mtanzania hasa mkulima mdogo kupitia mfumo wa stakabadhi za ghala. Umeongeza ushindani, umeongeza uwazi, na umefanikiwa kuhakikisha kwamba tunalinda ubora wa mazao yetu."

‎Aidha, amesisitiza umuhimu wa ushirikiano na uwajibikaji katika utekelezaji wa mfumo huo kwa kusema, "Hatuwezi kufikia malengo kama hatuta lazimisha masoko yetu ambayo kimsingi ndiyo yanatumika kama ulinzi kwa wakulima wetu. Ni lazima kila mmoja ahakikishe tunabadilisha mind set ya Watanzania kuhusu suala zima la stakabadhi za ghala."

‎Mhe. Londo pia amewataka watumishi wa stakabadhi za ghala kusimamia ushirikiano wa karibu na sekta binafsi, akibainisha kuwa, "Hatuwezi kufanikisha bila ushiriki wa sekta binafsi katika utekelezaji wa shughuli za kila siku. Ni lazima tutaidentify stakeholders na kuwaratibu ili kufanikisha majukumu yetu."

‎Ameongeza kuwa, "Kama tukisubiri watumishi wa kutosha, hatutaweza kusimamia vizuri katika ngazi za halmashauri na usimamizi utakuwa hafifu."

‎Mhe. Denis Londo amehitimisha kwa kusema, "Na sisi tuna bahati kuwa tunatumikia nchi yetu na kuitendea haki Serikali yetu. Tutende haki Rais wetu. Kila mmoja akitimiza wajibu wake, tutafanikiwa."

‎Awali akizungumza Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala, Asangye Bangu,  amesema kuwa mfumo wa stakabadhi za ghala umeleta mafanikio makubwa katika miaka ishirini, ikiwemo kuboresha bei, kuongeza uzalishaji na ubora wa bidhaa. 

Aidha, amebainisha kuwa bidhaa kumi na nane sasa zinatekelezwa kupitia mfumo huu na mpango wa kuongeza bidhaa zisizo za kilimo kama mifugo, uvuvi, na madini unatekelezwa.

‎Aidha, amebainisha kuwa maadhimisho ya miaka ishirini yatafanyika mwezi wa 4,2026 , ambapo watashirikisha wadau waliokuwa wakifanya kazi pamoja na kuwapa elimu wanafunzi na wakulima kuhusu mfumo huo. 







Katika kuenzi siku ya kuzaliwa Rais, wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji (OR-MU), Mhe. Dkt. Pius Chaya, ameshiriki zoezi la upandaji miti katika Makao Makuu ya Ofisi hiyo, Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma.

Zoezi hilo ambalo limefanyika leo tarehe 27 Januari 2026 linaungana na jitihada za kitaifa zinazoendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali nchini kwa lengo la kuongeza uoto wa asili na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

“Natoa wito kwa wengine kuunga mkono juhudi za Mhe. Rais kwa kupanda miti ya kutosha katika mazingira yetu”. Amesema Dkt. Chaya.

Dkt. Chaya ameongeza kuwa, nchi zetu zinaathiliwa sana na matatizo ya ukame, na kukosekana kwa mvua, hivyo kupitia kampeni ya Mhe. Rais ya kuhamasisha upandaji miti ni hatua nzuri ambayo itaenda kuzitatua changamoto hizo.

Aidha, Mhe. Naibu Waziri, aliwaongoza wafanyakazi wa Ofisi hiyo kukata keki ikiwa ni Ishara ya kuadhimisha siku ya kuzaliwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, wakithamini na kutambua mchango wake katika kuleta maendeleo ya Taifa.

Sambamba na hilo, Mhe. Naibu Waziri alitumia fursa hiyo, kukagua jengo la Wizara linaloendelea kujengwa katika Mji wa Serikali Mtumba ambapo ujenzi wake umefikia asilimia zaidi ya 80 ya utekelezaji, Mhe. Dkt. Chaya amemwelekeza Mkandarasi kukamilisha na kukabidhi jengo hilo kwa mujibu wa mkataba.
Na. Peter Haule, WF, Dodoma

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Deogratius Luswetula (Mb) ameiagiza Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kuendelea kuongeza udhibiti wa mikopo yenye riba kubwa (mikopo umiza) ili wananchi wapate mikopo yenye tija.

Ametoa maagizo hayo bungeni jijini Dodoma, wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Viti Maalumu, Mhe. Dkt. Neema Peter Majule, aliyetaka kufahamu hatua zilizochukuliwa na Serikali kwa watu wanaojinufaisha kwa kutoza riba kubwa kwenye mikopo, hatua inayopunguza jitihada za Serikali za kuwakwamua wananchi kiuchumi hususani wanawake na vijana.

Mhe. Luswetula alisema kuwa Serikali imeanza kuchukua hatua kwa wote wanaokiuka taratibu zilizowekwa na Serikali za utoaji mikopo kwa kusitisha leseni zao na hatua nyingine za kisheria.

“Wizara ya Fedha imejipanga kuhakikisha taasisi zote zinazotoa mikopo zinafuata taratibu na tayari Serikali imeandaa rasimu ya kusimamia mikopo ya kidigitali inayotarajiwa kuanza kutekelezwa Mwaka wa Fedha 2026/2027”, alisema Mhe. Luswetula.

Akijibu swali la msingi kuhusu hatua zilizochukuliwa kudhibiti mikopo hatarishi inayotolewa na baadhi ya taasisi zisizo rasmi, Mhe. Luswetula alisema kuwa Serikali, BoT na wadau wengine, imechukua hatua mbalimbali za kudhibiti mikopo hatarishi yenye riba kubwa kwa kuendelea kutoa elimu kwa wananchi.

Alisema kuwa mikopo inapaswa kutolewa na watoa huduma wenye leseni kutoka BoT kwa mujibu wa Sheria ya Benki na Taasisi za Fedha ya Mwaka, 2006 pamoja na Sheria ya Huduma Ndogo za Fedha ya Mwaka, 2018.

Hatua nyingine iliyochukuliwa ni pamoja na kuwatambua na kuchukua hatua za kiutawala dhidi ya watoa mikopo wasioidhinishwa ambapo programu 69 za mikopo ya kidigitali zilizobainika kutoa mikopo bila leseni zilisitishwa na programu 126 zilifungiwa.

Vilevile kutoa Mwongozo maalum kwa watoa huduma za mikopo ya kidigitali ili kuhakikisha uwazi, uendeshaji wa kimaadili, utoaji wa taarifa kamili kuhusu gharama za mikopo pamoja na ulinzi wa watumiaji wa huduma za kifedha.

Mhe. Luswetula alilitaja eneo lingine kuwa ni pamoja na kuandaa rasimu ya kanuni za kusimamia mikopo ya kidigitali, ambazo zinatarajiwa kuanza mwaka wa fedha 2026/27 ambapo Kanuni hizo zinalenga kuimarisha udhibiti wa wakopeshaji wa kidijitali nchini Tanzania.

Aidha, Mhe. Luswetula alisema kuwa Serikali kupitia Wizara ya Fedha, imekuja na programu ya elimu ya fedha ya mwaka 2020/2021 hadi 2025/2026 ikiwa ni mpango maalum wa kutoa elimu kwa wananchi kwa makundi yote ambayo inalenga kuwawezesha wananchi kupata uelewa, maarifa na kuwajengea maarifa ya kusimamia mapato na matumizi na kufanya maamuzi sahihi katika kutumia huduma rasmi za kifedha.

Alisema kuwa Wizara ya Fedha kila mwaka imekuwa ikiadhimisha Wiki ya Huduma ya Fedha Kitaifa kuanzia mwaka 2021 na mwaka huu yamefanyika Jijini Tanga kuanzia Januari 21, lengo likiwa wananchi kupata elimu ya fedha.

Mhe. Luswetula alisema miongoni mwa Mikoa ambayo maadhimisho hayo yamefanyika kuanzia mwaka 2021 ni pamoja na Dar es Salaam, Arusha, Mwanza, Mbeya na sasa Tanga.

Hadi sasa takribani mikoa 16 imefikiwa na huduma ya elimu ya Fedha na zaidi ya wananchi 64,000 wamefikiwa ikiwa ni pamoja na wanawake 40,000 na wanaume 24,000 na Halmashauri 94.


Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Deogratius Luswetula (Mb) akiiagiza Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kuendelea kuongeza udhibiti wa mikopo yenye riba kubwa (mikopo umiza) wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Mhe. Dkt. Neema Peter Majule, aliyetaka kufahamu Serikali imechukua hatua gani kwa watu ambao wamejinufaisha kwa mikopo yenye riba kubwa, bungeni jijini Dodoma.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha)
Kamishna Mkuu wa TRA Bw. Yusuph Juma Mwenda amesema Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ameiwezesha TRA kupitia Idara ya Forodha na Ushuru wa Bidhaa kuimarisha ulinzi mipakani kwa kuweka mifumo na vifaa vya kisasa vya kufanyia kazi.

Akizungumza katika maadimisho ya siku ya Forodha Duniani Januari 26.2026 yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam amesema Rais Samia wamewezesha kununuliwa na kufungwa kwa Scanner za kisasa 57 ambazo zimeongeza udhibiti mipakani.

Amesema kupitia Scanner hizo 57 ambazo zimefungwa Bandarini, mipakani na katika viwanja vya ndege wameweza kuzuia bidhaa zisizoruhusiwq kujngia nchini na kudhibiti bidhaa zilizodhibitiwa kuingia nchini pamoja na kuokoa afya za watanzania dhidi ya bidhaa hatarishi.

"Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amekuwa mstari wa mbele kutupa miongozo na kutuwezesha kutekeleza majukumu yetu ya kuihudumia nchi, Tunamshukuru sana na tunamuahidi kuendelea kufanya kazi kwa juhudi na maarifa" amesema Mwenda.

Amesema mbali na kuiwezesha TRA kupitia uwekezaji mkubwa alioufanya katika Bandari ya Dar es Salaam na Bandari nyingine nchini umewezesha kuongezeka kwa mapato ya Forodha kutoka Bilioni 800 na kufikia Trilioni 1.200 na kufanya mchango wa Idara ya Forodha kwa makusanyo ya TRA kuwa asilimia 39 ya makusanyo yote jambo ambalo ni la kujivunia.

Amesema kwa upande wa teknolojia Rais Samia amewekeza kwenye mfumo wa TANCIS ambao umeboresha utendaji kazi wa Forodha na kuongeza ufanisi kwa kuwawezesha walipakodi kupata huduma kupitia mtandao.

Ametoa wito kwa watumishi wote wa TRA kuongeza ufanisi, juhudi na maarifa katika utendaji kazi wao wa kila siku huku akiwapongeza kwa kujituma na kuwezesha kukusanywa kwa kiwango kikubwa cha kodi ambacho hakikuwahi kukusanywa katika miongo iliyopita cha Sh. Trilioni 4.13 kilichorekodiwa mwezi Desemba 2025.


Farida Mangube, Morogoro

MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Morogoro imenza kutoa mafunzo ya matumizi ya Mfumo Jumuishi wa Usimamizi wa Kodi za Ndani (IDRAS) kwa wafanyabiashara na walipa kodi 344,712, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kuanza kutumika rasmi kwa mfumo huo mpya.

Akizungumza kwenye mafunzo ya IDRIS kwa washauri wa kodi na wahasibu kutoka taasisi mbalimba na Uma na binafsi Meneja wa TRA Mkoa wa Morogoro, Sylver Rutagwelera amewataka kuupokea, kuujifunza na kuuelewa vizuri mfumo wa IDRAS ili kuboresha utoaji wa huduma na kuongeza ufanisi wa makusanyo ya kodi.

Amesema kuwa mfumo huo unatarajiwa kuanza kutumika rasmi Februari 9, 2026 na utasimamia kodi zote za ndani kwa kutumia mfumo mmoja jumuishi unaolenga kurahisisha ulipaji wa kodi na kuongeza mapato ya ndani ya Serikali.

“Tupo katika hatua ya kutoa elimu ya matumizi ya mfumo huu. Tumeanza na watumishi wetu, sasa tupo na wahasibu pamoja na washauri wa kodi kutoka taasisi binafsi na za Serikali. Mafunzo haya yatachukua wiki nzima na baadaye tutahusisha wadau wengine zaidi,” amesema Rutagwelera.

Ameongeza kuwa mafunzo ya awali yaliwahusisha watumishi wote wa TRA wanaohusika na mfumo huo katika mkoa mzima, na sasa elimu hiyo imeanza kutolewa kwa wafanyabiashara katika wilaya zote za Mkoa wa Morogoro.

Rutagwelera amesema baada ya kukamilika kwa mafunzo ya ngazi ya mkoa, timu ya TRA Morogoro itafika katika wilaya zote kutoa elimu hiyo kwa walipa kodi, sambamba na elimu inayotolewa na maofisa wa wilaya, ili kuhakikisha kila mfanyabiashara anauelewa vizuri mfumo wa IDRAS.

“Tutafanya mafunzo haya hapa ofisini na pia tutawafuata walipa kodi huko walipo hadi pale walipa kodi wote watakapoweza kutumia mfumo huu kikamilifu, kwani tuna walipa kodi 344,712 mkoani Morogoro,” amesema.

Mafunzo hayo yametolewa na Afisa Mwandamizi wa Tehama Ernest Shirima kwa kushirikiana na maafisa wa usimamizi wa kodi John Magembe na Mohamed Mchekaje ambapo wamesema mfumo wa IDRAS utarahisisha zaidi ulipaji wa kodi, kupunguza msongamano wa walipa kodi katika majengo ya TRA na kuongeza ufanisi wa ukusanyaji wa mapato.

Mfumo wa IDRAS una moduli 17, ambapo moduli mbili tayari zinafanya kazi tangu mwaka jana, ambazo ni Moduli ya Magari (Motor Vehicle Module) na Moduli ya Leseni za Udereva (Driving Licence Module), Registration, Communication, Return Filing and Assessment, pamoja na Knowledge Management, ambazo zinatarajiwa kutumika hivi karibuni.

Frida Joseph ni moja wa washiriki wa mafunzo hayo mkoani Morogoro, amesema mfumo wa IDRAS utaongeza uwazi na urahisi kwa walipa kodi. “Mfumo huu utapunguza usumbufu wa kufika mara kwa mara ofisi za TRA, na utarahisisha sana kazi yetu ya kuwasaidia walipa kodi kutimiza wajibu wao kwa wakati,” amesema.





Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan,ametoa tuzo kwa Kampuni ya Bia ya Serengeti (SBL) ikiwa ni kutambua mchango mkubwa wa kampuni na wadau wengine katika juhudi zao za uhifadhi wa mazingira na kuliletea taifa maendeleo endelevu.

Tuzo hiyo ya kihistoria Pongezi ambao ni ya kwanza kwa SBL kutolewa  na kingozi mkuu wa nchi, zinaonesha dhamira ya dhati ya kampuni hiyo katika utekelezaji wa mipango ya Mazingira, Jamii na Utawala Bora (ESG).

Kupitia programu zake mbalimbali, SBL hadi sasa imefanikiwa:

* Kupanda miti zaidi ya 10,000 katika Kanda ya Kaskazini na Kanda ya Kati

* Kutekeleza miradi ya maji safi na salama zaidi ya 28 kwa jamii zinazozunguka maeneo yake ya uzalishaji

* Kuwekeza katika kilimo endelevu kwa kuunga mkono vijana zaidi ya 300 kupitia mpango wa Kilimo Viwanda

Aidha, SBL imeanzisha mpango wa Shamba ni Mali, unaolenga kuwapatia wakulima mbolea, mbegu bora, teknolojia ya kisasa na elimu ya kilimo, na lengo la kuwafikia wakulima zaidi ya 4,000 ifikapo mwaka 2030.

Utambuzi huu unaakisi mchango wa SBL kama mdau anayejali mazingira na kuthamini jamii anazozihudumia, sambamba na kuunga mkono ajenda ya Taifa ya maendeleo endelevu


 

TUME ya Uchunguzi wa Matukio ya Uvunjifu wa Amani yaliyojitokeza wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, leo Februari 27, 2026, imekutana na Mkuu wa Majeshi Mstaafu (CDF) Venance Mabeyo.

Mkutano huo wa Tume na Mabeyo umefanyika katika Ukumbi wa Tanganyika uliopo katika ofisi za Benki Kuu ya Tanzania (BoT) jijini, Dar es Salaam.

Miongoni mwa yaliyojadiliwa ni pamoja na namna matukio hayo yalivyoanza, athari zake kwa watu, mali na miundombinu pia ushauri wa namna ya kuondokana na matukio hayo.

Tume inaendelea kukutana na makundi mbalimbali wakiwemo waathirika wa Matukio hayo ikiwa na lengo la kupata  kiini cha chanzo cha matukio hayo na kuyawasilisha kwa ajili ya hatua zaidi.









Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu akiwa ameshiriki katika Mkutano wa Mawaziri wa Kazi Duniani (Global Labour Market Conference) unaofanyika Jijini Riyadh, Saudi Arabia tarehe 26 Januari, 2026.

*****************

Na: OWM (KAM) – Riyadh, Saudi Arabia

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Clement Sangu amesema Serikali imeendelea kuchukua hatua madhubuti za kuongeza fursa za ajira kwa vijana nchini ikiwemo kushirikiana na sekta binafsi pamoja na wadau wa maendeleo.

Aidha, Mhe. Sangu amesema ushirikiano huo umewezesha wadau wa Maendeleo na sekta binafsi kutoa nafasi mbalimbali za ajira kwa vijana wa Tanzania nje ya nchi, kutokana na uwezo na ujuzi walionao.

Amesema hayo wakati aliposhiriki katika Mkutano wa Mawaziri wa Kazi Duniani (Global Labour Market Conference) unaofanyika Jijini Riyadh, Saudi Arabia Januari 26, 2026.

Amesema, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imefungua vyuo vya ufundi stadi, ambavyo vinatoa mafunzo ya ujuzi kulingana na mahitaji ya soko la ajira. Ameongeza kuwa, Vyuo hivyo vimekuwa chachu ya kuwawezesha vijana kupata ujuzi wa vitendo, kukuza ubunifu kuongeza ajira.

Vilevile, Waziri Sangu ameseema Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano imeendelea kutekeleza Programu ya Taifa ya Ukuzaji Ujuzi ambapo kupitia Programu hiyo vijana wamekuwa wakipatiwa mafunzo kwa njia ya Uanagenzi yanayolenga kuwajengea uwezo wa kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji, kupunguza tatizo la ukosefu wa ajira, kuongeza kipato cha mtu binafsi na kuchangia katika ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Kadhalika, Mhe. Sangu ameshukuru viongozi wa nchi mbalimbali kwa kuendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania kwa kuongeza fursa zaidi za ajira kwa Watanzania.

Mkutano huo unawakutanisha Mawaziri wa Kazi kutoka nchi zaidi ya 45 duniani na wameweza kujadili na kuweka mikakati ya kushirikiana katika soko la ajira, kuongeza kazi za staha kwa Vijana kwa kuzingatia mchango wa sayansi na teknolojia.



Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu akiwa ameshiriki katika Mkutano wa Mawaziri wa Kazi Duniani (Global Labour Market Conference) unaofanyika Jijini Riyadh, Saudi Arabia tarehe 26 Januari, 2026.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Clement Sangu akifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zikiwasilishwa wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Mawaziri wa Kazi Duniani (Global Labour Market Conference) unaofanyika Jijini Riyadh, Saudi Arabia.
Na Munir Shemweta, WANMM


Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo na Naibu wake Mhe. Kaspar Mmuya leo Januari 27, 2026 wamewaongoza watumishi wa Wizara katika zoezi la upandaji miti kwenye Ofisi za Wizara zilizopo eneo la Mtumba jijini Dodoma ikiwa ni siku ya kitaifa ya kuhamasisha upandaji miti.

Zoezi hilo linaongozwa na Kaulimbiu “Kesho yetu inaanza na mti unaopandwa leo, Panda mti kwa maendeleo endelevu ya makazi.”

Katika kufanikisha zoezi hilo, Viongozi wa taasisi zilizo chini ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi; Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Tume ya Taifa ya Matumizi ya Ardhi, Vyuo vya Ardhi Morogoro (ARIMO) na kile cha Tabora (ARITA) pamoja na Ofisi za Ardhi za Mikoa zimeelekezwa kushiriki zoezi hilo kwa kupanda miti kwenye maeneo yao.

Akizungumza wakati wa zoezi hilo Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo amesema, wizara yake inashiriki zoezi la upandaji miti kuunga mkono juhudi za Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mwana mazingira namba moja kutunza mazingira hasa ikizingatiwa kuwa, leo Januari 27, 2026 ni siku yake ya kuzaliwa.

Waziri huyo wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi amewahamasisha watumishi wa sekta ya ardhi nchini pamoja na wananchi kwa ujumla kukumbuka kuwa miti ni uhai hivyo wapande miti na kuitunza kwa lengo la kumuunga mkono Rais akiwa mwanamazingira namba moja.

”Wakati tunasherekea siku ya kuzaliwa ya Mhe. Rais, yeye ni mwana mazingira namba moja tunamuunga mkono kwa vitendo kwa kuhakikisha tunapanda miti ikiwa ni juhudi za kutunza mazingira’’ amesema.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan ametoa wito kwa watanzania kuendelea kujenga utamaduni wa kulinda na kuhifadhi mazingira kwa hiari wakitambua kuwa ulinzi wa mazingira ni msingi wa uhai, maendeleo na Usalama wa taifa.

Zoezi hili ni ishara ya uwajibike na linatoa fursa kwa kila mmoja kwa nafasi na mahali alipo kushiriki katika kulinda na kuenzi mazingira kwa manufaa ya sasa na kizazi kijacho.Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (kulia) akipanda mti katika eneo la Ofisi za Wizara ya Ardhi Mtumba Jijini Dodoma tarehe 27 Januari 2026 ikiwa ni siku ya kitaifa ya kuhamasisha upandaji miti. Kushoto ni Katibu Mkuu Mhandisi Anthony Sanga.Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Kaspar Mmuya akipanda mti kwenye eneo la Ofisi ya Wizara ya Ardhi lililopo katika Mji wa Serikali Mtumba Jijini Dodoma tarehe 27 Januari 2026 ikiwa ni siku ya kitaifa ya kuhamasisha upandaji miti.
Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhandisi Anthony Sanga (Kushoto) akishiriki zoezi la kupanda miti lililoongozwa na Waziri wa Ardhi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo katika ofisi za Wizara katika mji wa Serikali Mtumba tarehe 27 Januari 2026. Kulia ni Mkurugenzi wa Sera na Mipango wa Wizara ya Ardhi Dkt. Netho Ndilito.
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Bi. Lucy Kabyemera (Kushoto) akishiriki zoezi la kupanda miti lililoongozwa na Waziri wa Ardhi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo katika ofisi za Wizara katika mji wa Serikali Mtumba.

Sehemu ya watumishi wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Makao Makuu, wakiwa katika zoezi la upandaji miti lililoongozwa na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi katika Ofisi za Wizara katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)


Na Saidi Lufune, Dodoma
SERIKALI imeweka vikosi vya kudumu vya Askari katika Kata za Bwiti na Mwakijembe kwa lengo la kuwawezesha askari Wanyamapori kuwahi mwitikio haraka katika matukio ya wanyamapori wakali na waharibifu wanapovamia maeneo ya wananchi.

Hayo yamesemwa na Mhe. Hamad Hassan Chande (Mb.), Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Bungeni jijini Dodoma alipokuwa akijibu swali la Mhe. Twaha Said Mwakioja (Mb.) aliyetaka kujua hatua zinazochukuliwa na Serikali katika kudhibiti Tembo wanaojeruhi na kuharibu mali majumbani na mashambani.

Amesema kuwa hatua hiyo ni mkakati wa kitaifa unaotekelezwa na Serikali katika kukabiliana na wanyamapori wakali na waharibifu sambamba na kutumia teknolojia za kisasa hasa visukuma mawimbi (GPS collars); ndege nyuki (Drones) pamoja na mabomu baridi katika kudhibiti wanyamapori wakali na waharibifu hususan tembo katika Wilaya ya Mkinga.

Halikadhalika wakati akijibu swali la Mhe. Edibily Kazala Kinyoma (Mb.) aliyetaka kujua Serikali ina mpango gani wa kuwalipa fidia Wananchi wa Kitongoji cha Katoto waliopisha Mradi wa Kitalu cha Makere Forest Reserve, Mhe. Chande amesema tayari Serikali imefanya tathmini ya kaya na makazi kwa wananchi wa kitongoji cha Katoto na kugawa eneo la ukubwa wa Hekta 4,446 katika kitongoji cha Nyantuku kijiji cha Kagerankanda ambapo kila kaya ilipewa eneo la kujenga la ukubwa wa mita 32 kwa 64 na hekari 3 kwa ajili ya shughuli za kilimo.

“Wananchi wa Katoto waliohamishwa walishapatiwa fidia ambayo ni ardhi kwa ajili ya makazi, kilimo na mifugo ikiwa ni pamoja na Serikali kuwapatia usafiri wa mali zao kipindi walichokuwa wanahama.

Hadi kufikia Mwezi Oktoba, 2025 uongozi wa Mkoa wa Kigoma kwa kushirikiana na uongozi wa Wilaya ya Kasulu ulifanikiwa kuhamisha wananchi wote kutoka kitongoji cha Katoto na kwenda kitongoji cha Nyantuku kijiji cha Kagerankanda.” Alisema Mhe. Chande.





Top News