NA Mwandsihi Wetu – Chato

Wataalamu kutoka katika Sekta zinazotekeleza Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP ) inayoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu wamekutana Mjini Chato Mkoani Geita tarehe 8 Juni 2026 kwa lengo la kufanyia mapitio mpango kazi wa Programu hiyo.

Akizungumza katika ufunguzi wa kikao kazi hicho, Mhandisi Enock Nyanda, Mkurugenzi Msaidizi sehemu ya Sekta za Uchumi na Uzalishaji Idara ya Tawala za Mikoa Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI alisema lengo la wataalam hao kukutana ni sehemu ya utekelezaji wa maagizo ya kikao cha Mawaziri kilichofanyika mapema mwezi Mei mwaka huu.
Katika kikao hicho pamoja na mambo mengine kiliwataka wataamu hao kufanya mapitio ya kiutendaji katika mpango kazi wa utekelezaj wa Programu hiyo ikiwa ni pamoja na kuwasilisha na kujadili kazi, mapitio ya bajeti sambamba na kufanya tathmini fupi ya kila utekelezaji wa Programu.

Aidha timu hiyo ya wataalam pia itaandaa shughuli zitakazotekelezwa na program kwa mwaka 2027 ilikuweza kufikia malengo pamoja na kutembelea maeneo ya utekelezaji wa Mradi ya Rubambagwe Wilayani Chato pamoja na Kilimi Wilayani Nzega Mkoani Tabora.

Sekta zinazotekeleza Progreamu ya kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) ni Pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Kilimo, Shirika la Uvuvi nchini TAFICO, Shirika la Uvuvi Zanzibar ZAFICO, Wizara ya uchumi wa Buluu na Uvuvi Zanzibar, Wakala wa Mbegu Nchini ASA, Taasisi ya Uthibiti wa Ubora wa Mbengu Nchini TOSCI na Taasisi ya utafiti wa Mbegu za Kilimo Nchini TARI



-Asisitiza Tsh Trilioni 1.2 zimewekezwa Kilimanjaro, sasa ni zamu ya mfumo wa Usambazaji.

MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Baraa, Stephen Wasira, ameiagiza Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Same (SAUWASA) kuhakikisha inatatua kwa haraka changamoto ya upatikanaji maji inayowakabili wananchi wa mji wa Same.

Wasira alitoa agizo hilo leo Juni 8, 2026 alipokuwa akizungumza na wanachama wa CCM wa Shina Namba 9, Tawi la Same, Kata ya Same, wilayani Same mkoani Kilimanjaro.

Akijibu malalamiko ya wananchi kuhusu ukosefu wa maji, alisema haikubaliki kwa wakazi wa Same kuendelea kukosa huduma hiyo muhimu wakati maji yanapatikana kwa wingi kupitia miradi iliyotekelezwa na serikali.

“Ninaiagiza SAUWASA kuhakikisha wananchi wa Same wanapata maji. Haiwezekani watu wa Same waendelee kuyasikia au kuyaona maji bila kuyapata kwa matumizi yao ya kila siku, mfumo wa usambazaji uharakishwe ili wananchi wanufaike na huduma hiyo muhimu,” alisema Wasira.

Alibainisha kuwa, serikali imewekeza fedha nyingi kutekeleza mradi wa maji wa Same–Mwanga–Korogwe, hivyo hakuna sababu ya wananchi kuendelea kukosa huduma hiyo kutokana na changamoto za usambazaji.













NA MWANDISHI WETU

KAMATI ya Kudumu ya Bunge Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) imempongeza Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, kwa ujenzi wa  shule za kisasa za ghorofa  wilayani Ilala na kueleza kwa mara ya kwanza kamat hiyo imeshuhudia  jengo la shule ya sekondari ya kata yenye lifti.

Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa kamati hiyo  Florent Kyombo, katika ziara ya wajumbe wa kamati hiyo kukagua miradi  ya maendeleo katika Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaa, hususan ujenzi  wa  Shule ya  Sekondari ya Bonyokwa  itakayo chukua wanafunzi wa kidato cha tano na sita.

Kyombo amesema  kamati yake imezunguka mikoa mingi Tanzania lakini haijawahi kukutana na  jengo la shule lenye  hadhi  kama hilo la Shule ya Sekondari Bonyokwa lenye lifti.

"Jiji la Dar es Salaam wameupiga mwingi. Msione vinaelea viumeundwa. Tumezunguka mikoa mingi lakini hatujakutana na jengo lenye hadhi kama hii,"ameeleza  Mbunge Kyombo.

Amesema  kamati hiyo inamshukuru Rais Dk. Samia, kwa uwekezaji mkubwa katika sekta ya elimu hususan ujenzi wa shule za ghorofa ambao utaondoa adha kwa wanafunzi.

"Kamati inawaomba wanafunzi kumlipa Rais Dk. Samia, kwa kufanya vizuri  darasani na  kutunza mundombinu hii,"amebainisha  Kyombo.

Ameongeza  licha ya kutembelea na kukagua jengo hilo  la shule lakini maelezo ya awali  ya viongozi wa wilaya ya Ilala na Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam yanadhihirisha ujenzi  wa majengo mengi ya ghorofa hivyo kupongeza viongozi kwa utekelezaji wa miradi hiyo .

Hata hivyo kamati hiyo ilielekeza  halmashauri hiyo kuboresha majengo ya Shule ya Msingi Bonyokwa na Shule ya Sekondari Bonyokwa ya kiadato cha kwanza na cha nne, yawiane kidogo na hadhi ya jengo hilo la kissa.

Mbali na mradi huo, kamati hiyo mekagua  ujenzi wa Barabara ya Kwa mpalange (Buza) Temeke-Kitunda unaogharimu  kilometa 6.2, ujenzi wa Kituo cha Afya Mchikichini unaotekelezwa katika Kata ya Mchikichini unaogharimu sh. bilioni 7.4.

Awali Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, alimshukuru Rais Dk. Samia, kwa kuelekeza fedha nyingi za miradi wilayani humo na kwamba wataendelea  kusimamia kikamilifu kuhakikisha miradi hiyo inakamilika kwa wakati

Mpogolo, ameeleza  ujenzi wa shule za ghorofa ni mkakati uliwekwa kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo  2050 na kusimamia maono ya Rais Dk. Samia, wanafunzi wanasoma katika mazingira rafiki.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam,Elihuruma  Mabelya,  amesema  katika mwaka wa fedha 2026-27  wametenga sh. bilioni 19 kuboresha mundombinu ya elimu.

Mabelya amesema   mradi wa ujenzi wa Shule ya Sekondari Bonyokwa  umegharimu sh. bilioni 2.07  na ina madarasa 20, matundu ya vyoo 45 yakijumuisha matundu ya vyoo vya kawaida 30, matundu ya watu wennye mahitaji maalum 10, sehemu za  kujisaidia haja ndogo tano kwa wavulana, vyumba vitano  maaluma kwa wasichana vyenye choo ndani yake

"Shule hii inatarajia kuchukua wanafunzi 1400 mwaka 2026/27 na mwaka  mwaka 2028  shule  itachukua wanafunzi 3100,"amesema Mabelya.

Mbali na jengo la Shule ya Sekondari Bonyokwa kuwa na lifti  shule nyingine  ambayo jengo lake lina lifti wilayani humo ni Shule ya Sekondari  Kipunguni B.






Na Mwandishi wetu, DODOMA

Wanafunzi wanaojiandaa kushiriki mashindano ya Umoja wa Michezo na Taaluma kwa Shule za Sekondari Tanzania (UMMISETA) ngazi ya mkoa wamepata hamasa mpya baada ya kupokea vifaa vya michezo vilivyotolewa na Mbunge wa Jimbo la Mtumba, Anthony Peter Mavunde.

Vifaa hivyo vilikabidhiwa katika Shule ya Sekondari Dodoma kwa niaba ya Mbunge huyo kupitia Katibu wake, Silas Makanyaga, ambae alisema kuwa Jiji la Dodoma kupitia Ofisi ya Afisa Elimu Sekondari liliwasilisha ombi la vifaa vya michezo kwa ajili ya mashindano ya UMMISETA ngazi ya wilaya na mkoa, ambapo Mbunge amejitoa kusaidia kwa kununua jezi kwa kila mchezo.

“Tunawaomba vijana wetu kucheza kwa nidhamu, kuwasikiliza walimu wao na kuendelea kufanya vizuri kama ilivyo desturi ya Jiji la Dodoma ambalo limeendelea kuwa kinara kwa ushindi wa makombe mbalimbali” alisema Makanyaga.

Kwa upande, Afisa Elimu Sekondari Jiji la Dodoma, Mwl. Daniel Mapilya alisema kuwa tayari wanafunzi 120 kutoka shule mbalimbali za sekondari wamewasili kambini tangu Juni 5 kwa ajili ya maandalizi ya mashindano ya ngazi ya mkoa yaliyotarajiwa kuanza rasmi Juni 8. 

“Vijana hao wameonyesha utayari mkubwa wa kushiriki na kuonesha ushindani wa hali ya juu. Tumepokea vifaa mbalimbali ikiwemo jezi ambazo zimeongeza ari na furaha kwa wanafunzi wetu. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Mbunge kwa kuendelea kusimama nasi na mchango wake mkubwa katika maendeleo ya michezo” alisema Mwl. Mapilya.

Sambamba na hilo, Afisa Michezo wa Jiji la Dodoma, Peter Ititi alisema kuwa vifaa vilivyotolewa vimeongeza morali na hamasa kwa wanamichezo, akibainisha kuwa kwa miaka minne mfululizo mbunge huyo amekuwa akiwaunga mkono kwa kutoa vifaa vya michezo jambo lililosaidia kuongeza ushindani na mafanikio.

Nae, mchezaji wa mchezo wa kurusha tufe na Mpira wa Pete, Munira Mohamed alisema kuwa vifaa walivyopokea kutoka kwa mbunge vimeongeza hamasa na kuwapa nguvu ya kupambana kwa ushindi.

Hata hivyo, Nahodha wa timu ya mpira wa miguu, Gabriel Peter alisema kuwa timu ipo katika maandalizi mazuri na watapeperusha vizuri bendera ya Jiji la Dodoma kwa kurudi na ushindi mnono wa makombe kama zawadi ya shukurani kwa mbunge.

Mashindano ya UMISETA ngazi ya mkoa kwa Jiji la Dodoma yanashirikisha michezo mbalimbali ikiwemo mpira wa miguu (football), mpira wa pete (Netball), mpira wa kikapu (Basketball), mpira wa mikono (Handball), mpira wa wavu (Volleyball), riadha, sanaa za ndani, muziki wa kizazi kipya, tenisi ya mezani (Table Tennis), Goalball, kwaya na ngoma za asili.






 

Na Mwandishi wetu, Mirerani 
MADINI ya Tanzanite ya thamani ya zaidi ya shilingi milioni 993 yameuzwa kwenye minada miwili iliyofanyika hivi karibuni katika jengo la Tanzanite Exchange Centre mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara.

Afisa madini mkazi Mirerani (RMO) George Kaseza, ameyasema hayo kwenye ziara ya Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo Kenani Laban Kihongosi alipotembelea jengo hilo na kukagua akiwa ameongozana na viongozi wa mkoa na wilaya.

Kaseza amesema minada miwili ilifanyika hivi karibuni ambapo mnada wa kwanza wa mabroka ulifanyika Mei 15 mwaka 2026 kwa washiriki 84 na madini ya shilingi 271,270,100 yalinunuliwa.

"Mnada wa pili wa dealers ulifanyika Mei 21 mwaka 2026 na madini ya thamani ya shilingi 721,750,000 yalinunuliwa," amesema RMO Kaseza.

Amesema jengo la Tanzanite Exchange Centre linamilikiwa na Halamshauri ya Wilaya ya Simanjiro ila linaendeshwa na Tume ya Madini kupitia ofisi yake.

Katibu wa NEC, Itikadi Uenezi na Mafunzo Kenani Laban Kilongosi amewapongeza watumishi wa ofisi ya RMO Mirerani kwa namna wanavyofanya kazi katika eneo hilo.

Kenani amesema tayari soko hilo limeanza kuonyesha matokeo chanya ya uwekezaji huo kutokana na mwitikio mkubwa wa wafanyabiashara na mafanikio ya minada iliyofanyika ndani ya muda mfupi tangu kuanza kutumika.





WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amehitimisha ziara yake ya kikazi mkoani Iringa kwa kuwataka viongozi na watumishi wa umma kuendelea kusimamia haki, uwajibikaji na utoaji wa huduma bora kwa wananchi pamoja na kufuatilia utekelezaji wa maelekezo yote yaliyotolewa katika kutatua kero za wananchi.

Ametoa maelekezo hayo leo Jumapili (Juni 7, 2026) wakati akifunga ziara yake ya kikazi mkoani Iringa kwa kufanya kikao cha majumuisho na viongozi pamoja na watumishi wa umma kilichofanyika katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa.

Dkt. Mwigulu amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imewekeza fedha nyingi katika sekta mbalimbali za maendeleo hivyo ni wajibu wa viongozi na watumishi kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na haki zao zinalindwa.

Amesema ameridhishwa na namna Mkoa wa Iringa ulivyoshughulikia changamoto mbalimbali za wananchi na kuwataka viongozi kuendelea kuwa mbele ya matukio kwa kusikiliza na kutatua kero kabla hazijafikia hatua kubwa.

“Nimeona viongozi wa Mkoa wa Iringa wako mbele ya matukio. Kila hoja iliyojitokeza tayari ilikuwa imepokelewa na hatua mbalimbali zilikuwa zimeanza kuchukuliwa. Huo ndiyo mwelekeo ambao Serikali inautaka,” alisema.

Waziri Mkuu aliwataka viongozi wa Mkoa huo kufuatilia moja baada ya nyingine kero zote zilizowasilishwa katika ziara yake na kuhakikisha wananchi wanapata mrejesho wa hatua zinazochukuliwa.

Alisema Serikali itaendelea kufanya tathmini ya utekelezaji wa maelekezo hayo na kwamba viongozi wa mikoa na halmashauri wanapaswa kuweka kumbukumbu za utekelezaji wa kila hoja iliyowasilishwa na wananchi.

Katika sekta ya afya, Dkt. Mwigulu alisisitiza umuhimu wa kuhakikisha dawa muhimu na vifaa tiba vinapatikana kulingana na mahitaji ya maeneo husika pamoja na kuimarisha usimamizi wa fedha zinazotengwa kwa ajili ya huduma za afya.

Aidha, alizitaka halmashauri na taasisi za umma kuendelea kuwasaidia watu wenye ulemavu, wazee wasiojiweza na makundi mengine maalum kwa kutumia rasilimali zilizopo ili kuboresha ustawi wao.

Kwa upande wa miundombinu, Waziri Mkuu alielekeza kuharakishwa kwa utekelezaji wa miradi ya barabara iliyo katika hatua mbalimbali za maandalizi na utekelezaji huku akisisitiza ujenzi wa miundombinu yenye viwango vinavyoweza kuhimili changamoto za mazingira.

Pia aliwataka viongozi kuendelea kutatua migogoro ya ardhi kwa haki na kwa kuzingatia sheria pamoja na kuhimiza wananchi kurasimisha umiliki wa mali zao ili kuepusha migogoro inayoweza kujitokeza baadaye.

Akizungumzia utendaji wa watumishi wa umma, Dkt. Mwigulu alisema ni muhimu kuwatambua na kuwathamini watumishi wanaofanya kazi kwa uadilifu na ufanisi huku hatua stahiki zikichukuliwa kwa wale wanaoshindwa kutekeleza wajibu wao.

“Haki, uwajibikaji na huduma bora kwa wananchi lazima viwe msingi wa utendaji wetu. Wananchi wanatarajia kuona matokeo ya kazi zetu na ndiyo dhamira ya Serikali,” alisema.

Aidha, Waziri Mkuu aliwataka viongozi wa mkoa huo kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa maelekezo yote aliyoyatoa katika ziara hiyo ikiwemo migogoro ya ardhi, madai ya wananchi dhidi ya taasisi na kampuni mbalimbali, pamoja na masuala ya ustawi wa jamii yaliyowasilishwa katika mikutano ya hadhara.

Awali, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Kheri James alisema ziara ya Waziri Mkuu imeimarisha ari ya uwajibikaji kwa viongozi na watumishi wa umma pamoja na kutoa mwelekeo wa kushughulikia changamoto zinazowakabili wananchi katika maeneo mbalimbali ya Mkoa huo.











Mwamvua Mwinyi, Bagamoyo Juni 7,2026
JESHI la Polisi Mkoa wa Pwani limeanza uchunguzi wa kina kufuatia malalamiko ya mwanamke mmoja mkazi wa Gongo la Mboto, Dar es Salaam, anayodai kubadilishiwa mtoto baada ya kujifungua kwa njia ya upasuaji katika Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo.

Akitoa ufafanuzi kuhusu tukio hilo, kamanda wa Polisi mkoani Pwani,Salim Morcase alimtaja mlalamikaji huyo kuwa ni Filomena Richard Mataris (36), ambaye pamoja na mume wake, Carlos Kapata, walifika Kituo cha Polisi Bagamoyo Juni 5, 2026 na kutoa taarifa ya madai hayo.

Kwa mujibu wa Morcase, Filomena alihamia Kerege wilayani Bagamoyo Aprili 14, 2026 kwa ndugu yake Avetha Mabadiliko kwa ajili ya kupata uangalizi wa karibu wakati wa ujauzito.

"Mei 17, 2026 alipata uchungu wa kujifungua na kupelekwa Hospitali ya Kerege, ambapo baada ya kufanyiwa uchunguzi alibainika kuwa na dalili za uzazi pingamizi na kuhamishiwa Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo kwa ajili ya upasuaji."

" Mei 18, 2026 majira ya saa 8:30 usiku, Filomena alijifungua mtoto wa kiume kwa njia ya upasuaji na kudai kuwa alimwona na kumbeba mtoto huyo akiwa mzima wa afya, baada ya kuhamishiwa wodini, alidai kuoneshwa picha ya mtoto kupitia simu ya daktari na kuambiwa kuwa ndiye mtoto wake aliyefariki dunia.

Mama huyo alifafanua kuwa mtoto aliyeoneshwa kwenye picha alikuwa na changamoto mbalimbali za kiafya ikiwemo kichwa kilichobonyea na uvimbe kifuani, hali ambayo alisema ilikuwa tofauti na mtoto aliyemuona mara baada ya kujifungua.

Aidha, Filomena alidai kuwa aliambiwa mwili wa mtoto huyo ulikwishakabidhiwa kwa ndugu zake kwa ajili ya mazishi, bila yeye wala baba wa mtoto kushirikishwa au kufahamishwa kuhusu taratibu hizo.

Katika hatua za awali za uchunguzi, Kaimu Mganga Mkuu wa Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo, Dk. Mariam Ngwele, alieleza kuwa mtoto aliyezaliwa alikuwa na matatizo ya kiafya ikiwemo kichwa kilichobonyea, uvimbe kifuani na changamoto za upumuaji.

Dk. Ngwele, anasema mtoto huyo alifariki muda mfupi baada ya kuzaliwa licha ya jitihada za kitabibu zilizofanyika.

Na Mwandishi wetu, Mirerani 


MADINI ya Tanzanite ya thamani ya zaidi ya shilingi milioni 993 yameuzwa kwenye minada miwili iliyofanyika hivi karibuni katika jengo la Tanzanite Exchange Centre mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara.

Afisa madini mkazi Mirerani (RMO) George Kaseza, ameyasema hayo kwenye ziara ya Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo Kenani Laban Kihongosi alipotembelea jengo hilo na kukagua akiwa ameongozana na viongozi wa mkoa na wilaya.

Kaseza amesema minada miwili ilifanyika hivi karibuni ambapo mnada wa kwanza wa mabroka ulifanyika Mei 15 mwaka 2026 kwa washiriki 84 na madini ya shilingi 271,270,100 yalinunuliwa.

"Mnada wa pili wa dealers ulifanyika Mei 21 mwaka 2026 na madini ya thamani ya shilingi 721,750,000 yalinunuliwa," amesema RMO Kaseza.

Amesema jengo la Tanzanite Exchange Centre linamilikiwa na Halamshauri ya Wilaya ya Simanjiro ila linaendeshwa na Tume ya Madini kupitia ofisi yake.

Katibu wa NEC, Itikadi Uenezi na Mafunzo Kenani Laban Kilongosi amewapongeza watumishi wa ofisi ya RMO Mirerani kwa namna wanavyofanya kazi katika eneo hilo.

Kenani amesema tayari soko hilo limeanza kuonyesha matokeo chanya ya uwekezaji huo kutokana na mwitikio mkubwa wa wafanyabiashara na mafanikio ya minada iliyofanyika ndani ya muda mfupi tangu kuanza kutumika.


Na Mwandishi wetu – Dar es Salaam

SERIKALI kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) imeingia Makubaliano ya Ushirikiano (MoU) na Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam (DIT) yenye lengo la kuimarisha usimamizi wa maafa nchini kwa kutumia sayansi, teknolojia na ubunifu.

Akizungumza mapema hii leo (08 Juni, 2026) katika hafla ya utiaji saini wa makubaliano hayo Katibu Mkuu wa ofisi hiyo, Dkt. Jim Yonazi, amesema hatua hiyo ni utekelezaji wa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kujenga mifumo madhubuti ya kiutendaji inayoongozwa na maarifa, sayansi na teknolojia ikiwemo matumizi ya Akili Unde (AI) katika kukabiliana na maafa.

Amesema makubaliano hayo yanatekeleza pia mapendekezo ya Mkutano wa Nane wa Umoja wa Mataifa wa Jukwaa la Dunia la Upunguzaji wa Vihatarishi vya Maafa uliofanyika Geneva, Uswisi, mwezi Juni 2025, na yanaashiria mabadiliko ya kimkakati katika namna Serikali inavyoshughulikia changamoto za maafa kutoka mfumo wa kusubiri majanga hadi mfumo wa kujikita katika kinga, maandalizi na tahadhari.

“Vyuo vikuu na taasisi za utafiti, ikiwemo Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam, zina jukumu muhimu la kuzalisha maarifa na suluhisho za kisayansi zitakazosaidia kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa nchini,”amesema.

Ameongeza kuwa ili kuhakikisha utekelezaji madhubuti wa makubaliano hayo, Serikali itaandaa Mpango Kazi wa utekelezaji pamoja na Agenda ya Kitaifa ya Utafiti wa Usimamizi wa Maafa itakayobainisha maeneo ya kipaumbele yanayohitaji ufumbuzi wa kisayansi na kiteknolojia.

Dkt. Yonazi amesisitiza kuwa mafanikio ya makubaliano hayo yatapimwa kwa matokeo halisi yatakayochangia kuongeza usalama wa wananchi, kulinda rasilimali za taifa na kuimarisha ustahimilivu wa jamii dhidi ya maafa.

Ushirikiano huo unaendana na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayoweka msisitizo katika matumizi ya sayansi, teknolojia na ubunifu kama nguzo kuu ya maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii.

Kwa upande wake Mkuu wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam Prof.Preksedis Marco Ndomba amesema kuwa taasisi imeandika historia kwa kusaini hati ya ushirikiano na Ofisi ya Waziri Mkuu ambapo ameeleza kuwa mchakato huu ulianza muda mrefu na matunda yake yameanza kuonekana jambo ambalo ni mafanikio makubwa.

“Tunaahidi juu ya kufanikisha makubaliano hayo kwa kuwa, uwezo huo tunao, utalaam upo wa kutosha kwa kushirikiana kwenye masuala ya viatarishi kitaifa ili kufanikisha adhima hii ya Serikali,” Alisema Profesa Ndomba.













Bagamoyo, Juni 5, 2026.
HALMASHAURI ya Wilaya ya Bagamoyo imetoa wito kwa wadau wa maendeleo kuimarisha ushirikiano na serikali katika kuboresha miundombinu ya elimu na kuendeleza uhifadhi wa mazingira shuleni ili kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa wanafunzi.

Wito huo ulitolewa Alhamisi wakati wa zoezi la kupanda miti lililoandaliwa na Airtel Tanzania chini ya udhamini wa Airtel Africa Foundation katika Shule ya Msingi Kiromo iliyopo Wilayani Bagamoyo, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani.

Akizungumza kwa niaba ya Afisa Elimu wa Wilaya ya Bagamoyo, Hamis Kimenya ambaye ni Mkuu wa Kitengo cha Michezo, Utamaduni na Sanaa Halmashauri ya Mji wa Bagamoyo aliipongeza Airtel Tanzania kwa kushirikia na Airtel Africa Foundation kwa kuendelea kuisaidia Shule ya Msingi Kiromo na kuwahimiza wadau wengine wa sekta binafsi kujiunga na juhudi hizo zinazolenga kuboresha elimu na kulinda mazingira.

Alisema juhudi za uhifadhi wa mazingira, hasa upandaji miti, zinachangia kwa kiasi kikubwa kuboresha maeneo ya shule, kuongeza uoto wa kijani, kutoa kivuli, na kutengeneza mazingira yenye afya na yanayofaa zaidi kwa ujifunzaji.

“Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo inaendelea kujitolea kuweka mazingira wezeshi ya ushirikiano kati ya serikali na sekta binafsi, hasa katika sekta ya elimu. Tunahimiza wadau wengi zaidi kuunga mkono shule na jitihada za uhifadhi wa mazingira,” alisema.

Mkurugenzi Mtendaji wa Airtel Tanzania, Charles Kamoto, alisema Siku ya Mazingira Duniani inakumbusha ulimwengu kuwa ulinzi wa mazingira ni jukumu la pamoja linalohitaji hatua za pamoja kutoka kwa serikali, taasisi binafsi na jamii.

Alisema mpango wa kampuni hiyo wa kupanda miti katika Shule ya Msingi Kiromo unaonyesha dhamira yake ya muda mrefu katika uendelevu wa mazingira na maendeleo ya jamii.

“Leo hatupandi miti tu; tunawekeza katika mazingira yetu, jamii zetu, na vizazi vyajavyo,” alisema Kamoto. “Miti hii ya matunda itasaidia kulinda ardhi, kuboresha ubora wa hewa, kutoa kivuli, na baadaye kutoa matunda yatakayowanufaisha wanafunzi na jamii inayozunguka.”

Kamoto aliongeza kuwa mpango huo unaenda sambamba na maono ya Taasisi ya Airtel Africa (Airtel Africa Foundation) kupitia mpango wake wa “Adopt a School”, (Shule Yetu) ambao unasaidia uendelezaji wa mazingira salama, ya kijani, jumuishi na wezeshi ya kujifunzia kwa watoto kote Afrika.

Alibainisha kuwa Airtel imeendelea kuongeza juhudi za uhifadhi wa mazingira, akigusia kuwa mwaka jana kampuni hiyo ilifanya zoezi la kusafisha fukwe katika Fukwe ya Kawe jijini Dar es Salaam.

Mwaka huu, Airtel Tanzania imepanua juhudi zake kupitia upandaji miti katika Shule ya Msingi Kiromo, ikionyesha kuongezeka kwa dhamira ya uendelevu.

Katika hatua nyingine, mnamo Juni 5, 2026, Airtel pia ilifanya zoezi kubwa la kusafisha fukwe katika fukwe za Msasani na Kawe jijini Dar es Salaam kama sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani. Zoezi hilo lilisimamiwa na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC).

Akizungumza wakati wa usafi huo, Afisa Mazingira wa NEMC, Felician Kairuki aliwasihi wadau kuimarisha ushirikiano katika ulinzi wa mazingira kulingana na sera za kitaifa na mikakati ya usimamizi wa mazingira.

“Tunasisitiza umuhimu wa ushirikiano miongoni mwa wadau wote ili kuhakikisha mazingira yanalindwa kwa faida ya vizazi vya sasa na vijavyo,” alisema Kairuki.

Aliongeza kuwa ushirikiano endelevu kati ya taasisi za serikali, wadau wa sekta binafsi na jamii ni muhimu katika kukabiliana na changamoto za mazingira kama vile uchafuzi wa mazingira na usimamizi wa taka.

Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano wa Umma Airtel Tanzania, Jackson Mbando alisema kampuni hiyo imeendelea kutekeleza mipango mbalimbali ya uendelevu, ikiwa ni pamoja na kukuza suluhisho za kidijitali zinazopunguza utegemezi wa karatasi na vifaa vingine vinavyoweza kuchangia uharibifu wa mazingira.

Alisema hatua hizi ni sehemu ya dhamira pana ya Airtel ya kufanya biashara kwa masuala ya uwajibikaji na usimamizi wa mazingira.

Afisa Mtendaji wa Kata ya Kawe, Husna Nondo aliipongeza Airtel kwa kushiriki kikamilifu katika mazoezi ya kusafisha fukwe, akibainisha kuwa mamlaka za serikali za mitaa zinaendelea kuchukua hatua za kisheria dhidi ya watu binafsi na taasisi zinazochafua mazingira.

Alisisitiza kuwa ushirikiano kati ya serikali, sekta binafsi na jamii ni muhimu katika kuhakikisha kuwa fukwe, maeneo ya wazi na mazingira ya mijini yanabaki kuwa safi, salama na endelevu.

Mipango hiyo ya pamoja huko Bagamoyo na Dar es Salaam inaangazia ukuaji wa ushirikiano kati ya sekta binafsi, mashirika ya serikali na vyombo vya udhibiti katika kuendeleza uhifadhi wa mazingira, kukuza uendelevu na kuboresha ustawi wa jamii kote nchini Tanzania.

Top News