Wachezaji wa Timu ya Mpira wa Pete (Netiboli) ya Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na (Mazingira) wakiwa katika picha ya pamoja muda mfupi baada ya kuwasili katika Uwanja wa Amani Complex, Zanzibar kwa ajili ya uzinduzi rasmi wa Mashindano ya Ligi ya Muungano ya Mchezo Pete (Netiboli) iliyozinduliwa leo Alhamisi Januari 15, 2026.

******************

Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imesema itahakikisha uwepo wa Muungano wa Tanzania Bara na Zanzibar unaendelea kuimarika sambamba na kuibua fursa za ajira kupitia nyanja mbalimbali ikiwemo sekta ya michezo.

Hayo yamesemwa leo Alhamisi (Januari 15, 2026) na Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mhe. Ali Abdulgulam Ali wakati alipokuwa akizindua Ligi ya Taifa ya Muungano katika Uwanja wa Amani Complex, Zanzibar.

Mhe. Abdulgulam amesema michezo ni fursa ya ajira kwa vijana wa na hivyo Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar zitahakikisha zinatumia fursa hizo kuibua vipaji kwa vijana na kuwatengeneza ajira.

“Mashindano haya ni sehemu ya matunda ya Muungano uliojengwa kwa misingi umoja, amani na mshikamano….Serikali zote mbili zitahakikisha zinatumia fursa ya mashindano haya kuwezesha vijana kujitengenezea fursa za ajira” amesema Mhe. AbdulGulam.

Aidha amesema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar itahakikisha inaendelea kushirikiana na Chama cha Netiboli Zanzibar (CHANETA) na Chama cha Netiboli Tanzania (CHANETA)katika kuratibu mashindano hayo ili kuwa nguzo muhimu katika kukuza umoja, upendo na mshikamano kwa Watanzania.

Ameongeza kuwa Serikali zote mbili ztaendelea kuweka mazingira wezeshi kupitia sekta ya michezo ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya kisasa katika viwanja mbalimbali hatua inayolenga kuibua vipaji kwa vijana na kutengeneza ajira kwa Kundi hilo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Bi. Hanifa Selengiu amesema Serikali zote mbili zimeanzisha mashindano hayo kwa aijli ya kuhakikisha Watanzania wanaendelea kufahamishwa umuhimu wa Muungano na fursa zinazoibuliwa zilizopo ikiwemo sekta ya michezo.

“Mashindano ni utekelezaji wa maelekezo ya Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyotoa mwaka 2024 kuhusu jukumu ilioipatia Ofisi ya Makamu wa Rais ya kuutangaza Muungano” amesema Selengu.

Amesema Michezo ni sehemu muhimu ya Muungano na hivyo mashindano hayo yamekuja katika wakati mwafaka hususani katika kipindi hiki ambacho Serikali imekuwa mstari wa mbele katika kutoa elimu kwa umma kuhusu Muungano kwa makundi mbalimbali ikiwemo vijana.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Netiboli Zanzibar (CHANEZA) Bi. Nasra Juma amesema mashindano hayo yameshirikisha jumla ya timu 11 ikiwemo timu sita (06)kutoka Tanzania Bara na tano (05) kutoka Zanzibar.

Amezitaja timu hizo kuwa ni Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Uhamiaji, Tamisemi, Kikosi cha Kujitolea Zanzibar (KVZ), Afya- Zanzibar, Jeshi la Zimamoto, Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) Mbweni, Taasisi ya Uhasibu Arusha (IAA), Polisi Dodoma, Mafunzo na Jeshi la Kujenga Uchumi (JKU).

Amesema Chama hizo kimeendelea kuweka mikakati mbalimbali katika kuhakikisha Ligi ya ya Netiboli ya Muungano itaendelea kupata washiriki wengi zaidi kwani mchezo huo kwa sasa umezidi kukua na kuweza kufungua milango ya fursa za ajira kwa vijana.

Katika michezo iliyochezwa mapema leo asubuhi Timu ya JKU iliwezesha kupata ushindi wa magoli 36 kwa 34 dhidi ya Polisi Arusha wakati Mafunzo Zanzibar iliiadhibu Timu ya Afya Zanzibar kwa magoli 79 kwa 24.

Watendaji Waandamizi wa Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira)wakifuatilia matukio mbalimbali ya hafla ya uzinduzi Mashindano ya Ligi ya Muungano ya Pete iliyozinduliwa leo Alhamisi Januari 15, 2026. Aliyesimama ni Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Muungano Ofisi ya Makamu wa Rais Zanzibar, Bi. Shumbana Taufiq.
Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Muungano Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Bi. Hanifa Selengu akiwasilisha salamu za Uongozi wa Ofisi hiyo wakati wa hafla ya uzinduzi wa mashindano ya Ligi ya Muungano ya Mchezo wa Pete (Netiboli) iliyozinduliwa leo Alhamisi Januari 15, 2026.
Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Muungano Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Bi. Cecilia Nkwamu akifuatilia matukio mbalimbali ya hafla ya uzinduzi wa Mashindano ya Ligi ya Muungano ya Mchezo wa Pete (Netiboli)yaliyozinduliwa leo Alhamisi Januari 15, 2026.


Wachezaji wa Timu ya Mpira wa Pete (Netiboli) ya Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) wakipita mbele ya Mgeni rasmi Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mhe. Ali Abdulgulam Hussein muda mfupi kabla ya kuzinduliwa kwa wa Mashindano ya Ligi ya Muungano ya Mchezo wa Pete (Netiboli) iliyozinduliwa leo Alhamisi Januari 15, 2026.

Wachezaji wa Timu ya Mpira wa Pete (Netiboli) ya Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) wakipita mbele ya Mgeni rasmi Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mhe. Ali Abdulgulam Hussein muda mfupi kabla ya kuzinduliwa kwa wa Mashindano ya Ligi ya Muungano ya Mchezo wa Pete (Netiboli) iliyozinduliwa leo Alhamisi Januari 15, 2026.

Wachezaji wa Timu ya Mpira wa Pete (Netiboli) ya Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) wakiingia katika wa ndani wa Amani Complex, Zanzibar kwa ajili ya kwa ajili ya uzinduzi rasmi wa Mashindano ya Ligi ya Muungano ya Mchezo wa Pete (Netiboli) iliyozinduliwa leo Alhamisi Januari 15, 2026.

Wachezaji wa Timu ya Mpira wa Pete (Netiboli) ya Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) wakiwa pamoja na wachezaji wa Timu mbalimbali zinazoshiriki mashindano ya Ligi ya Muungano ya Mchezo wa Pete (Netiboli)iliyozinduliwa leo Alhamisi Januari 15, 2026.

Mke wa Rais wa Zanzibar, Msarifu na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Zanzibar Maisha Bora Foundation (ZMBF), Mama Mariam H. Mwinyi, leo tarehe 16 Januari 2026, ametembelea Shamba la Ngano la Mleiha Wheat Farm jijini Sharjah, shamba lenye zaidi ya ekari 2,000 linaloendeshwa kwa kutumia teknolojia za kisasa za kilimo.

Katika ziara hiyo, Mama Mariam alipata fursa ya kujifunza kwa vitendo kuhusu kilimo janja (AI Smart Agriculture), ikiwemo matumizi ya vihisi vya udongo vinavyosimamiwa kupitia programu za akili bandia (AI), kituo cha udhibiti, maabara pamoja na kitengo cha utafiti na maendeleo (R&D). Mafunzo hayo yalitolewa na Mtafiti wa Kilimo, Jawahir Mohammed AlAbdool.

Mama Mariam H. Mwinyi alieleza kufurahishwa na mchakato mzima wa uzalishaji wa ngano bora unaotumia teknolojia, akisisitiza dhamira yake ya kuunga mkono na kuendeleza kilimo kinachotumia teknolojia, taarifa sahihi na ubunifu kwa ajili ya maendeleo endelevu ya sekta ya chakula.

Aidha, Mama Mariam H. Mwinyi alitembelea Mleiha Archaeological Centre, moja ya maeneo yenye thamani kubwa ya kihistoria duniani, ambayo ni sehemu ya Faya Palaeolandscape, eneo la Urithi wa Dunia la UNESCO lililoidhinishwa hivi karibuni.

Katika kituo hicho, alipata fursa ya kujionea ushahidi wa makazi ya binadamu wa kale kuanzia enzi ya mawe (takriban miaka 130,000 iliyopita), ikiwemo zana za mawe, mabaki ya makazi ya Neolithic pamoja na makaburi ya zamani, likiwemo kaburi kubwa la Umm an-Nar lenye umbo la duara la takriban miaka 4,000, pamoja na makaburi ya farasi na ngamia yanayoonesha tamaduni za kijamii na mila za mazishi za kale.

Ziara hiyo inaakisi dhamira ya Mama Mariam H. Mwinyi katika kujifunza, kuenzi urithi wa kihistoria na kuhamasisha matumizi ya teknolojia, ubunifu na maarifa kama nguzo muhimu za maendeleo endelevu.



















Na Khadija Kalilli,Kibaha
KAIMU Katibu Tawala wa Mkoa wa Pwani, Shangwe Twamala, amewataka Waheshimiwa Madiwani wa Halmashauri za Wilaya ya Kibaha na Chalinze kuimarisha usimamizi madhubuti wa rasilimali za umma, ikiwemo mapato na fedha za Serikali, pamoja na kuhakikisha miradi ya maendeleo inatekelezwa kwa kuzingatia thamani ya fedha ili kuongeza tija na manufaa kwa wananchi.

Akizungumza leo Januari 16, 2026, wakati wa kuhitimisha mafunzo elekezi ya kuwajengea uwezo madiwani hao, Twamala amesema mafunzo hayo yamelenga kuwawezesha madiwani kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi, ili kuleta matokeo chanya yanayoonekana moja kwa moja kwa wananchi. Alisisitiza kuwa Serikali inatarajia kuona mabadiliko ya kweli yatokanayo na maarifa na ujuzi walioupata kupitia mafunzo hayo.

Ameeleza kuwa madiwani wanapaswa kuzingatia misingi ya utawala bora, kuheshimu sheria, kanuni na taratibu, pamoja na kusimamia kikamilifu utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa kuzingatia vipaumbele vya Serikali, hususan katika kuboresha huduma za kijamii na kuchochea ukuaji wa uchumi katika sekta mbalimbali.

Aidha, amewataka madiwani hao kutafsiri kwa vitendo vipaumbele vya Serikali kupitia utekelezaji wenye tija wa majukumu yao, huku wakizingatia maslahi mapana ya wananchi wanaowawakilisha.

Katika hatua nyingine, Twamala amesisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya madiwani, wataalamu na wananchi, sambamba na kuepuka migogoro isiyo ya lazima inayoweza kukwamisha maendeleo. Ameongeza kuwa madiwani wanapaswa kuzingatia utu, utulivu, kujitawala kihisia na kusikiliza kwa makini kero na changamoto za wananchi ili kuzitatua kwa busara.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Mafunzo hayo, Mhe. Hasani Mwinyikondo, Diwani wa Kata ya Msoga, amesema mafunzo hayo yamewajengea uwezo mkubwa madiwani katika utekelezaji wa majukumu yao, hususan kwenye usimamizi wa miradi ya maendeleo, fedha za umma na masuala ya utawala bora.

Mhe. Mwinyikondo amebainisha kuwa mada zilizotolewa ni pamoja na uongozi na utawala bora, sheria na taratibu za uendeshaji wa shughuli za Serikali za Mitaa, uendeshaji wa vikao, uandaaji wa mipango na bajeti, usimamizi na udhibiti wa fedha, usimamizi wa rasilimali watu, haki na stahiki za viongozi, pamoja na maadili ya uongozi.

Mafunzo hayo yanatarajiwa kuwa chachu ya kuimarisha utendaji wa madiwani na kuongeza ufanisi katika kusimamia maendeleo na utoaji wa huduma bora kwa wananchi wa Halmashauri za Wilaya ya Kibaha na Chalinze.


Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Januari 16, 2026 ameongoza kikao cha kimkakati na Mawaziri, Naibu Mawaziri, Makatibu Wakuu wa kisekta, Ofisini kwake, Mlimwa Jijini Dodoma.

Katika kikao hicho, viongozi hao wamejadili kuhusu changamoto za biashara kati ya Tanzania na Zambia

Wizara zilizohudhuria kikao hicho ni pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu ( Sera Bunge na Uratibu), Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji, Wizara ya Fedha, Wizara ya Nishati, Wizara ya Uchukuzi, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Pia, kikao hicho kilihudhuriwa na Wakuu wa Mikoa ya Mbeya, Songwe na Rukwa.







Na. Saidina Msangi na Joseph Mahumi, WF, Dodoma.

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amekutana na kufanya mazungumzo kwa nyakati tofauti na Balozi wa Japan nchini Tanzania, Mhe. Yoichi Mikami na Mkurugenzi Mkazi wa Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD), Bw. Sakphouseth Meng, ambapo wamejadili namna ya kuimarisha zaidi ushirikiano kupitia utekelezaji wa miradi ya kimkakati ikiwemo nishati na kilimo.

Akiwa na Balozi wa Japan, Mhe. Balozi Omar aliishukuru nchi hiyo kwa kuendelea kushirikiana na Tanzania katika nyanja mbalimbali za kiuchumi na kijamii kwa kusaidia utaalam, mikopo nafuu na misaada ya kiufundi ambayo imeisadia Tanzania kupiga hatua kupitia sekta za kilimo, elimu, na viwanda.

Aidha, Mhe. Balozi Omar aliwaalika wawekezaji kutoka Japan kuja kuwekeza nchini Tanzania katika sekta mbalimbali zenye kuleta tija kwa pande zote mbili.

Kwa upande wake Balozi wa Japan nchini Tanzania, Mhe. Yoichi Mikami, ameipongeza Serikali ya Tanzania kwa kuendelea kuimarisha ushirikiano na nchi yake, na kwamba kuna idadi kubwa ya Wajapan, waliowekeza na kutaka kuja kuwekeza nchini Tanzania na kuiomba Serikali iendelee kuboresha mazingira ya uwekezaji ili kuvutia wawekezaji wengi zaidi.

Katika Tukio lingine, Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Omar, aliushukuru Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo IFAD kwa kuwekeza dola za Marekani bilioni 2 tangu uanze kushirikiana na Tanzania katika kukuza kilimo, nishati na miradi mingine ya kijamii.

Alimweleza Mkurugenzi Mkazi wa Mfuko Huo nchini Tanzania Mhe. Sakphouseth Meng, kwamba Tanzania inaukaribisha mpango mpya wa 14 wa Mfuko huo utakaotekelezwa nchini ambapo Mfuko huo unatarajia kuwekeza kati ya dola za Marekani milioni 60 hadi milioni 70 kwenye maeneo ya kilimo, nishati, miundombinu katika maeneo ya vijijini.

‘‘Tanzania inafurahia ushirikiano kati yake na IFAD ambao umeanza muda mrefu tangu mwaka 1978 na tumekubaliana kuimarisha ushirikiano huu, kwa kuangalia zaidi maeneo yanayohitaji rasilimali kwa kutumia taasisi za fedha za ndani ikiwemo Benki yetu ya Maendeleo ya Kilimo TADB ambayo imekuwa ikifanya vizuri’’, alisema Mhe. Balozi Omar.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkazi wa Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo-IFAD, nchini Tanzania, Bw. Sakphouseth Meng, aliipongeza Serikali kupitia Wizara ya Fedha kwa kuendeelea kusimamia vizuri uchumi wa nchi na kwamba IFAD itaendelea kuwekeza zaidi katika sekta za kiuchumi na kijamii kupitia mpango wake wa kuwainua wananchi masikini wanaoishi maeneo ya vijijini.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (kulia), akiagana na Balozi wa Japan nchini Tanzania, Mhe. Yoichi Mikami, aliyefika kwa ajili ya kujitambulisha na kujadili masuala mbalimbali ya ushirikiano wa kiuchumi na maendeleo kati ya Tanzania na Japan, katika Ofisi ya Waziri wa Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akizungumza jambo wakati wa kikao chake na Balozi wa Japan nchini Tanzania, Mhe. Yoichi Mikami (hayupo pichani), aliyefika kwa ajili ya kujitambulisha na kujadili masuala mbalimbali ya ushirikiano wa kiuchumi na maendeleo kati ya Tanzania na Japan, katika Ofisi ya Waziri wa Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.
Balozi wa Japan nchini Tanzania, Mhe. Yoichi Mikami, akizungumza jambo wakati wa kikao chake na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), alipofika kwa ajili ya kujitambulisha na kujadili masuala mbalimbali ya ushirikiano wa kiuchumi na maendeleo kati ya Tanzania na Japan, katika Ofisi ya Waziri wa Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (Katikati), Balozi wa Japan nchini Tanzania, Mhe. Yoichi Mikami (wa tatu kushoto), Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb)(wa tatu kulia), Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Bi. Amina Khamis Shaaban (wa pili kulia), Kaimu Kamishna wa Idara ya Uchambuzi wa Sera, Wizara ya Fedha, Dkt. Remidius Ruhinduka (wa pili kushoto), Afisa wa Siasa, Utamaduni na Uhusiano wa Umma, ubalozi wa Japan nchini, Bi. Yoshino Shibata (kushoto) na Afisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Frank Mhina (kulia), wakiwa katika picha ya pamoja, baada ya kikao cha Mhe. Balozi Omar na Mhe. Mikami, kilichofanyika katika ofisi za Wizara ya Fedha, Treasury Square jijini Dodoma
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (kulia), akiagana na Mkurugenzi Mkazi wa Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD), Bw. Sakphouseth Meng, baada ya kukutana na kufanya mazungumzo katika ofisi za Wizara ya Fedha, Treasury Square jijini Dodoma, ambapo pamoja na mambo mengine Mhe. Balozi Omar, aliishukuru IFAD kwa mchango wake katika maendeleo ya kilimo nchini.

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akizungumza jambo wakati wa kikao chake na Mkurugenzi Mkazi wa Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD), Bw. Sakphouseth Meng (hayupo pichani), katika ofisi za Wizara ya Fedha, Treasury Square jijini Dodoma, ambapo wawili hao walijadiliana masuala mbalimbali ya ushirikiano katika kukuza maendeleo ya Sekta ya kilimo na miundombinu ya nishati.
Mkurugenzi Mkazi wa Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD), Bw. Sakphouseth Meng, akizungumza jambo wakati wa kikao chake na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), (hayupo pichani), katika ofisi za Wizara ya Fedha, Treasury Square jijini Dodoma, ambapo wawili hao walijadiliana masuala mbalimbali ya ushirikiano katika kukuza maendeleo ya Sekta ya kilimo na kuongeza tija katika sekta hiyo.

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (katikati), akizungumza jambo wakati wa kikao chake na Mkurugenzi Mkazi wa Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD), Bw. Sakphouseth Meng (hayupo pichani), katika ofisi za Wizara ya Fedha, Treasury Square jijini Dodoma, ambacho kilijadili masuala mbalimbali ya ushirikiano katika kukuza maendeleo ya Sekta ya kilimo kwa ujumla wake na kwa upande wa kuongeza uzalishaji na tija katika uzalishaji. Wengine katika picha ni Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb)(Kushoto) na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Bi. Amina Khamis Shaaban (Kulia).
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (Kulia), akiteta jambo na Mkurugenzi Mkazi wa Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD), Bw. Sakphouseth Meng, wakati wakibadilishana kadi kwa ajili ya mawasiliano baada ya kikao chao kilichofanyika katika ofisi za Wizara ya Fedha, Treasury Square jijini Dodoma, ambacho kilijadili masuala mbalimbali ya ushirikiano katika kukuza maendeleo ya Sekta ya kilimo kwa ujumla wake na kwa upande wa kuongeza uzalishaji na tija katika kilimo.
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb)(Kulia) akiteta jambo na Mkurugenzi Mkazi wa Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD), Bw. Sakphouseth Meng, baada ya kikao cha Mkurugenzi huyo na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), kilichofanyika katika ofisi za Wizara ya Fedha, Treasury Square jijini Dodoma.  
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (Katikati), Mkurugenzi Mkazi wa Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD), Bw. Sakphouseth Meng, wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kikao chao kilichofanyika katika Ofisi za Wizara ya Fedha, Treasury Square jijini Dodoma. Wengine katika picha ni Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (wa nne kulia), Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Bi. Amina Khamis Shaaban (wa tatu kushoto), Kamishna Msaidizi wa Idara ya Usimamizi wa Madeni, Wizara ya Fedha, Bw. Omary Khama (wa pili kulia), Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Sheria, Wizara ya Fedha, Bi. Zawadi Maginga (kulia), Mratibu Mkazi wa IFAD, Bi. Jacqueline Machangu-Motcho (wa tatu kulia), Wachumi kutoka Idara ya Fedha za Nje Wizara ya Fedha, Bw. John Kuchaka (wa pili kushoto) na Bi. Zahra Michuzi (kushoto).

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Dodoma)


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni ya kitaifa ya uhamasishaji uwekezaji wa ndani kwa mwaka 2026. Uzinduzi huo umefanyika leo Januari 16, 2026 jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA) Gilead Teri, akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni ya kitaifa ya uhamasishaji uwekezaji wa ndani kwa mwaka 2026. Uzinduzi huo umefanyika leo Januari 16, 2026 jijini Dar es Salaam.


SERIKALI imewataka Watanzania kutumia ardhi wanayomiliki kama mtaji wa kuingia kwenye uwekezaji, badala ya kuiacha bila kuendelezwa, hatua itakayosaidia kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.

Wito huo umetolewa leo Januari 16, 2026 jijini Dar es Salaam na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, wakati wa uzinduzi wa kampeni ya kitaifa ya uhamasishaji uwekezaji wa ndani kwa mwaka 2026.

Profesa Kitila amesema moja ya maeneo muhimu yatakayofanyiwa kazi kupitia kampeni hiyo ni suala la ardhi, akieleza kuwa Watanzania wengi wanamiliki maeneo makubwa ya ardhi lakini hawana uelewa wa namna ya kuyatumia kiuchumi.

Amesema kupitia Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA), wananchi watapatiwa elimu juu ya namna ya kuyakabidhi maeneo yao kwa mamlaka hiyo ili kusaidiwa kupata wawekezaji watakaowekeza katika ardhi hizo kwa mfumo wa ubia au makubaliano rasmi.

“Lengo ni kuwasaidia Watanzania kubadilisha ardhi yao kuwa mali yenye thamani, inayoweza kuleta ajira, mapato na maendeleo endelevu,” amesema Profesa Kitila.

Ameongeza kuwa serikali itaendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji ili kuwahamasisha Watanzania kutumia rasilimali walizonazo, ikiwemo ardhi, kama nyenzo ya kushiriki kikamilifu katika uchumi wa nchi sambamba na uwekezaji wa wageni.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Masoko kutoka Benki ya Equity, Shumbana Walwa amesema ufadhili na ushirikiano kati ya benki hiyo na Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA) utaleta manufaa makubwa kwa Watanzania, hususan katika kuwawezesha wawekezaji wa ndani kupata mitaji na huduma za kifedha kwa urahisi.

Amesema kupitia ushirikiano huo, Benki ya Equity itaendelea kutoa elimu ya kifedha, ushauri na bidhaa mbalimbali za kifedha zitakazowawezesha Watanzania kubadilisha mawazo yao ya kibiashara kuwa miradi halisi ya uwekezaji.

Ameongeza kuwa ushirikiano huo utasaidia kuongeza ushiriki wa Watanzania katika uwekezaji wa ndani, kukuza biashara ndogo za kati na Kubwa pamoja na kuchochea maendeleo ya uchumi wa nchi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TISEZA, Gilead Teri, amesema mamlaka hiyo imejipanga kuzunguka mikoa yote ya Tanzania Bara na Zanzibar kwa kushirikiana na Benki ya Equity, kwa lengo la kutoa elimu ya uwekezaji na kuwaunganisha wamiliki wa ardhi na wawekezaji wa ndani na nje ya nchi.

Teri amesema kwa mwaka 2026, TISEZA inalenga kusajili miradi 1,500 ya uwekezaji, ambapo sehemu kubwa inalenga kuwahusisha Watanzania moja kwa moja kupitia umiliki wa ardhi na miradi ya ubia.

Amebainisha kuwa juhudi hizo ni sehemu ya mageuzi makubwa ya sekta ya uwekezaji chini ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, yenye lengo la kuwawezesha Watanzania kiuchumi na kuongeza ushiriki wao katika uwekezaji.

Kwa upande wake, mwekezaji wa ndani, Willium Ngeleja, amesema uzinduzi wa kampeni hiyo utakuwa na manufaa makubwa kwa Watanzania, kwani utaongeza uelewa juu ya fursa za uwekezaji zilizopo nchini na kuwahamasisha wananchi kushiriki moja kwa moja katika shughuli za kiuchumi.

Ngeleja amesema kampeni hiyo itasaidia kubadilisha mtazamo wa Watanzania kuhusu uwekezaji, hasa kwa kuwa itatoa elimu ya kina kuhusu taratibu, vivutio na namna ya kuanza kuwekeza hata kwa mtaji mdogo.

Ameongeza kuwa jitihada za serikali katika kuhamasisha uwekezaji wa ndani zitachochea ukuaji wa uchumi, kuongeza ajira na kuimarisha ushiriki wa wazawa katika miradi mikubwa ya maendeleo nchini.






Matukio mbalimbali.

Top News