Na Farida Mangube
Mbunge wa Jimbo la Ulanga, Salim Alaudin Hashim, ameiomba Serikali kuharakisha ujenzi wa kipande cha barabara ya Lupiro–Mahenge, akisema ni muhimu kwa usafirishaji wa mazao ya kilimo na madini katika Wilaya za Ulanga na Malinyi, Mkoa wa Morogoro.
Ametoa ombi hilo wakati wa hafla ya kumkabidhi mkandarasi kazi ya ujenzi wa Daraja la Namuhanga lililopo Tarafa ya Lupiro. Daraja hilo lilisombwa na mafuriko, jambo lililosababisha usumbufu mkubwa kwa wananchi wa Wilaya za Ulanga na Malinyi.
Mbunge Salim amesema ana imani ujenzi wa daraja hilo utakamilika kwa wakati kabla ya kuanza kwa msimu ujao wa mvua, ili kurahisisha shughuli za kiuchumi, hasa kilimo ambacho ndicho tegemeo kuu la wananchi wa maeneo hayo.
«“Tunashukuru sana Serikali kwa kutuona sisi wananchi wa Wilaya za Ulanga na Malinyi. Wananchi sasa wanaenda kuondokana na adha iliyokuwa ikiwapata kutokana na kusombwa kwa Daraja la Namuhanga,” amesema Mbunge Salim.»
Kwa upande wake, Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, amesema Mkoa wa Morogoro ni miongoni mwa maeneo yenye changamoto kubwa za miundombinu ya barabara na madaraja, lakini Serikali imejipanga kuhakikisha changamoto hizo zinapatiwa ufumbuzi.
Akizungumzia mradi wa barabara ya Lupiro–Malinyi, Waziri Ulega amesema tayari fedha za ujenzi kwa kiwango cha lami zimetengwa na mkandarasi anatarajiwa kuanza kulipwa malipo ya awali wakati wowote ili kazi ianze rasmi.
"Nyinyi wakazi wa Wilaya hizi mbili ni wazalishaji wakuu wa chakula hapa nchini. Serikali imedhamiria kuhakikisha tunamaliza tatizo hili la miundombinu, hasa barabara ambazo zitajengwa kwa kiwango cha lami ili kuwaondolea changamoto za usafiri na usafirishaji,” amesema Waziri Ulega."
Ujenzi wa barabara na madaraja katika eneo hilo unatarajiwa kuongeza urahisi wa usafirishaji wa mazao, kuchochea biashara na kuimarisha maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi wa Ulanga na Malinyi.





.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)


.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)


.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)



.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)



.jpeg)




.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)

