Ofisi kiunganishi wa Mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro iliyopo Dodoma imeendelea kufikia makundi mbalimbali ya taasisi za umma na binafsi, shule pamoja na wadau mbalimbali kutoa elimu ya uhifadhi na utalii sambamba na kutangaza bidhaa za utalii zilizoko eneo la hifadhi ya Ngorongoro.

Kwa mujibu wa Mkuu wa Ofisi Kiunganishi ya Ngorongoro iliyoko Dodoma Afisa Uhifadhi Mkuu Lowaeli Damalu kazi ya kutoa elimu na kutangaza utalii wa ndani kwa mikoa ya kanda ya kati inayojumuisha Singida na Dodoma ni endelevu kuhakikisha kuwa elimu ya vivutio vya utalii na shughuli za uhifadhi katika eneo la Ngorongoro zinatangazwa hasa kwa wanafunzi na taasisi za elimu ambao ni mabalozi wazuri wa kurithisha vizazi ambavyo ndio jeshi la uhifadhi wa aliasili kwa siku zijazo

Kwa upande wake Afisa Elimu Maalum wa Jiji la Dodoma, Mwalimu Issa Kambi, ameeleza kuwa jitihada za Ngorongoro kuhamasisha utalii wa ndani na kuhimiza uhifadhi wa mazingira ni ishara ya kujali wanafunzi ambao ndio nguzo ya taifa la kesho.  Wanafunzi wa shule za Dodoma ikiwemo shukl ya msingi Dodoma Viziwi wametoa shukrani kwa Mamlaka ya Uhifadhi Ngorongoro kwa kuwatembelea na kuahidi kuwa mabalozi wa utunzaji wa mazingira na kutangaza vivutio vya utalii majumbani mwao.

Eneo la hifadhi ya Ngorongoro lina utitiri wa vivutio vya utalii vinavyojumuisha utalii wa kuona Wanyama, utalii wa picha, utalii wa malikale, miamba, jiolojia, misitu, ndege, mazingira. Wageni wanaofika Ngorongoro wanapata fursa ya kutembelea na kuona eneo la Olduvai na Laetoli ambayo yana gunduzi za masalia mbalimbali ya historia ya binadamu na mambo kale.







-Yaweka msisitizo ushirikishwaji wa Serikali za Mitaa kwenye miradi ya umeme

-Wasisitizwa kutekeleza mradi ndani ya wigo wa mkataba

-Wapewa maelekezo kufanya mradi kwa weledi na utaalamu

-Bilioni 6.6 kuunganisha wateja wa awali 1,929

Morogoro

Wakandarasi wanaotekelza miradi ya kusambaza umeme nchini wametakiwa kushirikiana kwa karibu na Viongozi wa Serikali za Mitaa ili utekelezaji wa miradi ya kupeleka umeme kwa wananchi iweze kuleta tija na kuchochea uchumi wa nchi.

Hayo yamezungumzwa na Meneja wa Usimamizi wa Miradi ya Kusambaza Umeme kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mha. Deogratius Nagu katika kikao maalum cha kwanza cha kufungua mradi wa kuwaunganishia umeme wananchi mkoani Morogoro (Last Milestone Connectivity Project ) ambacho kimehudhuriwa na Wataalam kutoka REA, TANESCO na Wakandarasi kampuni ya Magna Vis Group Ltd.

"Viongozi wa Serikali za mitaa wale ndio wenye maeneo husika na wale ndio watakayoonyesha maeneo tutakayowapeleka wananchi umeme kulingana na wigo uliopo kimkataba na hii itatusaidia sana kufikisha huduma za umeme kwa walengwa wa mradi" Amebainisha Mha. Nagu.

Katika hatua nyingine, Mha. Nagu ameeleza kuwa, mradi huo ni mahsusi katika kutekeleza mpango mkubwa wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuongeza watumiaji wa umeme nchini.

"Serikali imedhamiria kuunganisha takribani wananchi milioni 8.6 kuwezesha kupata huduma ya umeme ndani ya miaka mitano kuanzia mwaka 2025 hadi 2030 ambapo sisi REA tunatekeleza mpango huu kupitia miradi hii ya kuwaunganishia umeme wananchi, " Amesema Mha. Nagu.

Aidha, ameongeza kuwa Mkandarasi atekeleze mradi kwa weledi na kufuata taratibu za kimkataba na hivyo kupelekea mradi kukamilika kwa wakati na kuharakisha wananchi kupata huduma za nishati ya umeme kwa haraka.

Naye, Meneja wa TANESCO Mkoa wa Morogoro Kaskazini, Mha. Zawadi Macha amesisitiza ubora wa mradi kuzingatiwa katika kipindi chote cha mradi na kuhakikisha wanawapa taarifa ya mradi mara kwa mara viongozi wa Serikali za Mitaa ili kuwawezesha kufahamu hatua mbalimbali za utekelezaji zinazofikiwa.

Vile vile Mha. Msangi ameongeza kuwa, takribani shilingi bilioni 6.6 zimetolewa na Serikali ili kuunganisha wateja wa awali wapatao 1,929 katika Mkoa wa Morogoro kuweza kupata huduma ya umeme na hatimaye kuwawesesha kuendesha shughuli zao za kiuchumi ikiwemo kuchomelea na machine za kusaga zinazotumia umeme.

Halikadhalika Msimamizi wa mradi kutoka kampuni ya Magna Vis Group Ltd, Mha. James Kimaro amebainisha kuwa watazingatia taratibu zote zilizopo katika mradi ili ziende sambamba katika kipindi chote cha utekelezani wa mradi huo mkoani Morogoro.



Na John Mapepele, New York- Marekani.

Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa, amesema kuwa matumizi sahihi ya teknolojia na utafiti yana nafasi kubwa katika kushughulikia changamoto za idadi ya watu na kuharakisha maendeleo endelevu.

Akizungumza katika Mkutano wa 59 wa Idadi ya Watu na Maendeleo kinachofanyika New York nchini Marekani Aprili 13-17/ 2026, Mchengerwa amesema Tanzania inaendelea kuweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha kuwa mabadiliko ya kiteknolojia yanawanufaisha wananchi wote.

“Ni heshima kubwa kuhutubia mkutano huu kwa niaba ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” alisema Mchengerwa, akisisitiza kuwa serikali inapongeza mjadala wa kimataifa unaolenga kuunganisha teknolojia, utafiti na maendeleo ya watu.

Ameeleza kuwa Tanzania inatambua umuhimu wa kutumia vyema idadi kubwa ya vijana kama fursa ya kukuza uchumi.

“Kutumia kikamilifu nguvu ya vijana wetu ni msingi muhimu wa kufikia ukuaji wa uchumi jumuishi na endelevu,” alisisitiza.



Mheshimiwa Mchengerwa ameeleza kuwa, masuala ya idadi ya watu yamejumuishwa katika mipango ya maendeleo ya taifa ikiwemo Dira ya Maendeleo ya 2050 na Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Miaka Mitano, hatua inayolenga kuendana na Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs).

Katika hatua nyingine, Waziri huyo alibainisha mafanikio yaliyopatikana katika sekta ya teknolojia, akitaja upanuzi wa miundombinu ya kidijitali kupitia Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano na Mradi wa Tanzania ya Kidijitali. Alisema uwekezaji huo umeongeza upatikanaji wa huduma za serikali mtandao na kukuza ujuzi wa kidijitali hasa vijijini.

“Hatua hizi zinawezesha ushiriki mpana katika uchumi wa kidijitali huku tukihakikisha usalama wa taarifa na mifumo ya mawasiliano,” aliongeza.



Aidha, amesisitiza umuhimu wa takwimu sahihi katika kupanga maendeleo, akitaja mafanikio ya Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022 pamoja na maboresho ya mfumo wa usajili wa vizazi na vifo (CRVS).
Katika sekta ya afya, Mchengerwa alisema serikali inaendelea kutekeleza huduma ya afya kwa wote kupitia Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote ya mwaka 2023.

Aliongeza kuwa matumizi ya teknolojia kama tiba kwa njia ya mtandao na mifumo ya kidijitali yameboresha utoaji wa huduma.

“Tunaendelea pia kuboresha afya ya mama na mtoto kupitia uwekezaji katika huduma za uzazi salama na huduma za dharura,” alisema.



Kuhusu usawa wa kijinsia, Mchengerwa alisema serikali inaendelea kupambana na ukatili wa kijinsia na kuongeza ushiriki wa wanawake katika uchumi pamoja na sekta za sayansi na teknolojia.

Akizungumzia vijana, alieleza kuwa zaidi ya nusu ya Watanzania ni vijana, hivyo Serikali inawekeza katika elimu, ujuzi na ajira ili kunufaika na nguvu kazi hiyo.

“Tunaimarisha elimu ya sayansi na teknolojia pamoja na programu za ubunifu na ujasiriamali kwa vijana,” alisema.



Kwa upande wa ushirikiano wa kimataifa, Mchengerwa alitoa wito kwa nchi mbalimbali kuimarisha ushirikiano na kubadilishana teknolojia ili kusaidia nchi zinazoendelea.

“Tanzania iko tayari kushirikiana na wadau wote kuhakikisha maendeleo ya teknolojia yanaleta matokeo chanya kwa kizazi cha sasa na kijacho,” alisisitiza.

Alihitinisha kwa kusisitiza dhamira ya Tanzania ya kuhakikisha maendeleo jumuishi: “Tutaendelea kujitolea kuhakikisha hakuna mtu anayebaki nyuma.”






Anthony Mariki , katikati akipokea ufadhili wa kwenda kusoma chuo Kikuu cha Johannesburg Afrika kusini , Shahada ya Uhandisi wa Madini , kulia Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) , Profesa Willliam Anangisye na kushoto , Meneja Mkazi wa Kampuni ya Barrick Nchini, Dkt Melkiory Ngido



Anthony Maliki , wa kwanza kushoto waliosimama akiwa na wanafunzi wenzake waliopata ufadhili wa kwenda kusoma nchini Afrika Kusini Chuo cha Johannesburg, wakiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa Barrick na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) , waliokaa wa kwanza kushoto , Meneja Rasilimali Watu wa Barrick nchini , Lumbu Kumbula, Meneja Mkazi wa Barrick nchini , Dkt Melkiory Ngido, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa William Anangisye na wa kwanza kulia ni Mkuu wa Shule ya Madini na Jiolojia (SOMG) Profesa Elisante Mshiu.



**

“Nikiwa ni miongoni mwa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Johanesburg nchini Afrika ya Kusini nikisomea fani ya uhandisi wa madini kwa ufadhili wa kampuni ya Barrick Tanzania najivunia kuwa katika programu hii ya kuwapatia mafunzo wataalamu wa sekta ya madini wa siku zijazo na ninaamini ina manufaa makubwa kwa Tanzania ambayo ni nchi yenye hazina kubwa ya madini ya aina mbalimbali” anasema Antony Godfrey Mariki.

Godfrey Mariki ni miongoni mwa wanafunzi watano wa mwaka wa kwanza kutoka shule ya Madini na Sayansi ya Miamba (SoMG) katika Chuo Kikuu cha Dar es salaam walioshinda ufadhili (Scholarship) ya kampuni ya Barrick yenye ubia na Serikali ya Tanzania kupitia kampuni ya Twiga Minerals ambaye kwa sasa anasoma kozi ya uhandisi wa madini nchini Afrika ya Kusini.

Katika mahojiano yaliyofanyika karibuni kutokea nchini Afrika ya Kusini, Mariki amesema anayo furaha kuona yeye na wenzake wanaendelea vizuri katika masomo yao wakiwa wanapata msaada na ufuatiliaji wa karibu kutoka kwa mfadhili yaani kampuni ya Barrick na Chuo Kikuu cha Dar es salaam ambapo walikuwa wanasoma hapo awali.

”Ufadhili huu tuliopata naamini sio wa kifedha tu bali ni fursa ya kipekee ya kujiendeleza kitaaluma kwa kupata elimu bora kutoka chuo bora barani Afrika ikizingatiwa kuwa Afrika ya Kusini imeendelea zaidi katika sekta ya madini zaidi ya hapo katika vipindi vya likizo Barrick imetupatia fursa ya kupata mafunzo ya vitendo kwenye migodi yake ili tuweze kupata maarifa zaidi”,amesema Mariki.

Kuhusiana na progamu hii Mariki anasema kuwa Barrick imeonyesha maono yake kwa kuwekeza kwenye elimu inaolenga kuboresha sekta ya madini nchini Tazania “Kupitia program hii ni dhahiri kwamba Barrick inaanda waaalamu wazawa kutoka Tanzania watakaoendeleza na usimamia sekta ya madini katika siku za mbele ili kuhakikisha inatoa mchango mkubwa kwa ukuaji wa uchumi wa nchi sambamba na kuwanufaisha Watanzania”,amesema.

Mariki ameongeza kuwa anafurahi kuona Barrick mbali na kutoa ufadhili huu pia imekuwa na programu mbalimbali za mafunzo zinazolenga kuwajengea uwezo wataalamu wa sekta ya madini ikiwemo kuendesha semina za wanafunzi wanaosoma fani ya madini na utafii wa madini kwa kutumia wataalamu wa kampuni ambapo pia imekuwa ikitoa fursa kwa wanafunzi wa vyuo vikuu kupata mafunzo ya vitendo katika migodi yake ya North Mara na Bulyanhulu.

Akielezea historia yake fupi ya elimu amesema elimu ya msingi alisoma katika Shule ya Royal iliyopo mjini Moshi na alipomaliza alichaguliwa kujiunga na Seminari ya St,James nayo ipo mkoani Kilimanjaro baadaye masomo ya juu ya sekondari katika shule ya Kisimiri ambayo imemjenga zaidi katika safari ya kutimiza ndoto yake akaweza kupata vigezo vya kujiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kusomea kozi aliyoipenda ya uhandisi wa Madini.

Mariki anaamini kuwa mafanikio yoyote yanapatikana kwa kuwa na bidii katika jambo lolote ambalo mtu anafanya na kutoa wito kwa vijana wenzake nchini kuchangamkia fursa zinazojitokeza kuanzia kwenye masomo,kazi,biashara na shughuli nyinginezo zote."Mafanikio yoyote maishani yanahitaji kufanya kazi kwa bidii",amesisitiza.

Anasema wakati serikali ya Tanzania inakwenda kasi katika kutekeleza mipango mbalimbali ya maendeleo kwenye sekta mbalimbali ikiwemo sekta ya madini,kunahitajiwa uwekezaji wenye mipango mikubwa utakaowezesha miradi mbalimbali ya kimkakati inayoendelea kuanzishwa kuwa endelevu na sio tu kuwekeza kwenye fedha na teknolojia bali kuwekeza pia katika kupata wataalamu wa kuendesha miradi kwa kipindi cha sasa na miaka ya mbele.

Ameendelea kueleza kuwa kuwa bila kufanya uwekezaji wenye mtazamo wa kujenga biashara endelevu kwa miaka mingi, kuna hatari ya biashara nyingi hususani katika sekta nyeti kama za madini,usafirishaji na mafuta kuendelea kutegemea wataalamu wa kigeni na watanzania kuachwa nyuma na kubaki kama watazamaji.

Anashauri kuwa kuna haja ya kuwapatia vijana wengi wa kitanzania fursa za kusoma fani zenye wataalamu wachache katika vyuo vikuu vya ndani na nje ya nchi sambamba na kuanzishwa Progamu mbalimbali za kuwanoa vijana wa kitanzania wahitimu wa vyuo vikuu na vyuo vya ufundi kwa kuwapatia mafunzo ya vitendo kwa ajili ya kuwaanda kwendana na mabadiliko yanayotokea katika kila sekta na kushika nafasi za uongozi katika siku za usoni.

Akiongea kuhusu kupata nafasi ya Ufadhili wa Barrick kusomea taaluma ya madini nchini Afrika ya Kusini Mariki, anaeleza kuwa anajivunia kuwa miongoni mwa wanafunzi wachache waliochaguliwa kwa kuwa ushindani wa kuipata nafasi ulikuwa mkubwa sambamba na mchujo mkali uliofanywa na wataalamu mbalimbali ili kuhakikisha na kujiridhisha kuwa wanachukua watu wenye uwezo, makini na waliopo tayari kujifunza."Nina uhakika tutafanya vizuri na kupata kile kilicho bora na kukirudisha kwa taifa katika kutumikia watanzania wote kwa manufaa ya nchi ",amesisitiza.

Anasema moja ya ndoto kubwa aliyokuwa nayo katika maisha yake ni kufanya kazi katika kampuni kubwa na zenye mifumo mizuri ya kazi, jambo ambalo linaelekea kutimia kutokana na kampuni ya Barrick kutangaza pia fursa kuwapatia ajira pindi watakapomaliza elimu sambamba na kuwapatia mafunzo ya kuwajengea uwezo wa kufanya kazi kwa vitendo wakati wote watakapokuwa masomoni.

Kuhusu mambo yanayomvutia kutamani kufanya kazi katika kampuni ya Barrick amesema ni mengi mbali na kupata maslahi mazuri na utaalamu wa viwango vya kimataifa pia anavutiwa na jinsi inavyotekeleza mkakati wake endelevu wenye mtazamo wa kujenga jamii endelevu kwendana na utekelezaji wa malengo endelevu ya milenia ya umoja wa mataifa (MDGs).

"Inafurahisha kuona kampuni inayapa kipaumbele masuala ya msingi katika kujenga biashara endelevu kama vile utunzaji wa mazingira na vyanzo vya maji,usalama wa wafanyakazi wake ,kushirikiana na jamii zilizopo katika maeneo inakofanyia biashara zake kama ambavyo inafanya kazi na wazabuni wa ndani kuhakikisha inafanya manunuzi ya ndani ya nchini kwa asilimia kubwa ,kuendesha mafunzo ya ujasiriamali kwa wazabuni ili nao biashara zao zikuwe na kuwa endelevu bila kusahau kufanikisha miradi mbalimbali ya kusaidia jamii hususani katika sekta za elimu, ,afya, ,maji safi na salama na uboreshaji wa miundombinu ya barabara", amesema Samson.

Mariki, anaeleza kuwa anaamini kuwa hadi kufikia kuhitimu shahada yake ya kwanza nchini Afrika ya Kusini, atakuwa amejifunza mambo mengi yatakayomsaidia katika safari yake ndefu ya kuwa mtaalamu wa madini sambamba na kuwa mbunifu na kutoa mawazo ya kitaalamu yanayowezesha kukabili changamoto na kuwezesha sekta ya madini nchini Tanzania kusonga mbele kwa mafanikio makubwa.

Amemalizia kwa kutoa ushauri kwa wawekezaji wengine wanaotoka nje na ndani ya nchi kuiga mfano wa Barrick kwa kuwa na mtazamo wa kujenga biashara endelevu sambamba na kuwa na programu za kuandaa wataalamu wazawa kwa kuwawezesha kupata elimu na utaalamu kama ambavyo imedhamini wanafunzi watano kusomea utaalamu wa fani ya madini nje ya nchi.

"Programu kama hii ni muhimu kwa kuwanoa vijana wasomi kupata ujuzi wa viwango vya kimataifa ,natamani kuona pia idadi ya vijana wanaochukuliwa katika Programu hii kuongezwa zaidi ya sasa ili inufaishe vijana wengi wa kitanzania", amesisitiza.


Mbunge wa Jimbo la Ushetu, Mhe. Emmanuel Cherehani akizungumza na wananchi katika kijiji cha Mwabomba Kata ya Idahina Halmashauri ya Ushetu mkoani Shinyanga - Picha na Kadama Malunde

Mbunge wa Jimbo la Ushetu, Mhe. Emmanuel Cherehani akikaribishwa katika kijiji cha Mwabomba kata ya Idahina Halmashauri ya Ushetu mkoani Shinyanga.


Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog


Mbunge wa Jimbo la Ushetu, Mhe. Emmanuel Cherehani amefanya ziara muhimu ya kukagua na kuhimiza utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika Kata ya Idahina, Halmashauri ya Ushetu, sambamba na kufanya mkutano mkubwa wa shukrani kwa wananchi waliomchagua kuwa mbunge wao.


Katika ziara hiyo iliyofanyika leo Jumatatu Aprili 13, 2026 Mhe. Cherehani ametembelea Mradi wa Ujenzi wa Daraja la Mwabomba uliokamilika kwa asilimia 99 na tayari kuanza kutumika, pamoja na kuzindua rasmi ujenzi wa Kituo cha Afya Mwabomba (Idahina), hatua inayolenga kuboresha huduma za afya kwa wananchi wa eneo hilo.


Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika Kijiji cha Mwabomba, Mhe. Cherehani ametoa shukrani zake kwa wananchi pamoja na uongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinachoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan, akisisitiza dhamira yake ya kuwatumikia wananchi kwa uaminifu.

“Leo Aprili 13, 2026 ni siku ya kumbukumbu ya kuzaliwa kwangu, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uzima sote wananchi wa Ushetu. Nimekuja kusherehekea nanyi na kusema neno moja tu ‘Asante’. Asanteni sana kwa kunichagua kuwa Mbunge wenu na kwa kumchagua Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwa Rais na madiwani wa CCM” amesema Cherehani.


Mbunge huyo ameeleza kuwa serikali imetoa shilingi bilioni 2.2 kwa ajili ya ujenzi wa Daraja la Mwabomba, ambalo sasa limeanza kuwahudumia wananchi bila hofu, huku akitangaza kukabidhi shilingi milioni 657 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Idahina.


“Nimekuja kuwakabidhi kiasi cha shilingi milioni 657 kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya na wananchi wasichangishwe hata shilingi mia. Tayari milioni 250 zipo kwenye akaunti, nataka ujenzi uanze mara moja ili wananchi waanze kupata huduma,” amesisitiza.


Aidha, ametoa maagizo kwa watendaji wa sekta ya afya kuhakikisha huduma kwa wajawazito zinatolewa bila malipo, akipiga marufuku vitendo vya kuwatoza fedha.


“Ni marufuku kumtoza hata shilingi 10 mama mjamzito. Wapokeeni, wapimeni na wahudumieni. Hawa ni wananchi wa kawaida, wanashinda mashambani ,wanatoa wapi fedha?” amehoji.

Mbali na afya, Mhe. Cherehani amezungumzia mipango ya maendeleo ikiwemo upatikanaji wa maji kupitia mradi wa Ziwa Victoria, ufunguzi wa soko la dhahabu Mwabomba na utatuzi wa changamoto za wafugaji kupata maeneo ya malisho.


Katika mkutano huo, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga, Mabala Mlolwa aliyekuwa mgeni rasmi amempongeza Mhe. Cherehani kwa kusimamia kwa vitendo miradi ya maendeleo.

“Ushetu mna mbunge mchapakazi, mmelamba dume sana, ni mbunge wa Vitendo, Cherehani inashona maendeleo kweli kweli Ushetu. Ni vigumu kupata kiongozi mwenye upendo na jitihada kama hizi. Daraja la Mwabomba sasa linapitika, wananchi wanavuka bila hofu,” amesema Mlolwa.


Ameongeza kuwa miradi hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya CCM na maono ya Serikali ya kuwaletea wananchi maendeleo ya kweli, huku akihimiza wananchi kuendelea kudumisha amani, mshikamano na kuunga mkono serikali yao ili kuharakisha maendeleo zaidi.


Ameongeza kuwa wananchi wanapaswa kuendelea kuunga mkono juhudi za serikali na kudumisha amani, akibainisha kuwa maendeleo yanayoonekana ni matokeo ya sera na utekelezaji wa CCM chini ya uongozi wa Rais Samia.


Mradi wa Daraja la Mwabomba kwenye barabara ya Masumbwe–Mwabomba unaounganisha mikoa ya Shinyanga na Geita, umetekelezwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) kwa kushirikiana na mkandarasi M/s Jossam & Co. Ltd, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa maagizo ya Rais Samia kufuatia uharibifu wa miundombinu uliotokea hapo awali.
















Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ameutembelea mradi wa Mji wa AFCON Fumba uliopo Mkoa wa Mjini Magharibi.

Ziara hiyo imefanyika leo tarehe 14 Aprili 2026, akiambatana na Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Dkt. Riziki Pembe Juma, pamoja na wadau wa mradi wa AFCON Fumba Zanzibar.

Katika ziara hiyo, Rais Dkt. Mwinyi amekagua maeneo mbalimbali ya uwanja huo wa kisasa wa AFCON unaojengwa na kampuni ya ORKUN GROUP ya Uturuki, unaotarajiwa kutumika kwa michuano ya AFCON mwaka 2027 itakayofanyika kwa ushirikiano wa nchi tatu za Afrika Mashariki za Kenya, Uganda na Tanzania.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi ametembelea na kukagua miundombinu inayotarajiwa kujengwa kuzunguka uwanja huo, ikiwemo hospitali, barabara, migahawa, maduka makubwa (mall) pamoja na huduma nyingine muhimu zitakazouzunguka mji huo wa kisasa.

Uwanja huo unakadiriwa kuchukua watazamaji elfu 35, ukiwa na viwango vya ubora vinavyokubalika na Shirikisho la Soka Barani Afrika (CAF).









 



Na Oscar Assenga, Lushoto

Kampuni ya Taifa Gas imeendelea kuunga mkono juhudi za Serikali kuhamasisha matumizi ya Nishati Safi ya Kuikia huku ikijipambanua kama kinara wa usambazaji wa gesi nchini Tanzania, ikiwa na takribani asilimia 51 ya ujazo wa gesi yote inayopatikana nchini.

Akizungumza kuhusu mafanikio hayo wakati wa Tamasha la NMB Kijiji Day lilofanyika Magamba wilayani Lushoto, Meneja wa Masoko wa kampuni hiyo, Oscar Shelukindo, amesema kuwa mafanikio hayo yanatokana na uwekezaji mkubwa katika miundombinu ya kuhifadhi na kusambaza gesi, pamoja na dhamira ya dhati ya kuwahudumia Watanzania.

Ameeleza kuwa lengo kuu la kampuni hiyo ni kusaidia juhudi za taifa za kuhamasisha matumizi ya nishati safi, kwa kuwahamasisha wananchi kuachana na matumizi ya kuni na mkaa, ambayo yamekuwa na athari kubwa kwa afya na mazingira.



Kwa mujibu wa takwimu, zaidi ya Watanzania 33,000 hufariki kila mwaka kutokana na magonjwa yanayosababishwa na matumizi ya nishati zisizo safi.

Hali hiyo imeifanya Taifa Gas kuongeza juhudi za kuhakikisha gas inapatikana kwa urahisi na kwa gharama nafuu.

Katika hatua hiyo, kampuni hiyo inatoa mitungi ya gesi ya kilogramu 6 na 15 kwa bei nafuu, pamoja na huduma ya kujaza mitungi kwa wateja waliokwisha kuwa nayo, hatua inayolenga kuwafikia wananchi wengi zaidi.



Aidha, Taifa Gas kwa kushirikiana na NMB Bank wanatarajiwa kushiriki katika Tamasha la Kijiji Day, ambapo watatoa huduma mbalimbali pamoja na elimu kwa wananchi kuhusu matumizi sahihi ya nishati safi.





Juhudi hizi zinatajwa kuwa chachu ya mabadiliko chanya, zikilenga kuboresha afya za Watanzania na kulinda mazingira kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

 


Sehemu ya washiriki wa Mkutano wa Nne wa Wakaguzi wa ndani wa Taasisi na sekta za umma, ulioandaliwa na Taasisi ya Ukaguzi wa ndani nchini Tanzania (IIA), Mkoani Morogoro.

Rais na Mwenyekiti wa Bodi ya Taasisi ya Ukaguzi wa Ndani, Bw. Jonathan Ngoma akizungumza katika Mkutano wa Nne wa Wakaguzi wa ndani wa Taasisi na sekta za umma, ulioandaliwa na Taasisi ya Ukaguzi wa ndani nchini Tanzania (IIA), Mkoani Morogoro.

Sehemu ya washiriki wa Mkutano wa Nne wa Wakaguzi wa ndani wa Taasisi na sekta za umma, ulioandaliwa na Taasisi ya Ukaguzi wa ndani nchini Tanzania (IIA), Mkoani Morogoro.

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula akifungua Mkutano wa Nne wa Wakaguzi wa ndani wa Taasisi na sekta za umma, ulioandaliwa na Taasisi ya Ukaguzi wa ndani nchini Tanzania (IIA), Mkoani Morogoro.




Na Mwandishi Wetu, Morogoro

NAIBU Waziri wa Fedha, Bw. Laurent Luswetula amewataka wakaguzi wa Ndani wa taasisi na sekta za umma nchini kuongeza ufanisi kwa kazi zao na kuhakikisha wanakuwa huru ili fedha na rasilimali zinazotolewa na Serikali kwa jamii zitumike kama zilivyo tarajiwa.

Bw. Luswetula ameyasema hayo wakati akifungua mkutano wa nne wa wakaguzi wa ndani wa Taasisi na sekta za umma, ulioandaliwa na Taasisi ya Ukaguzi wa ndani nchini Tanzania (IIA), ambapo alisisitiza wakaguzi hao kuwa huru kwa kuwa wao ndio macho ya Serikali katika matumizi ya fedha kwa mashirika ya umma na miradi mbalimbali ya maendeleo nchini.

"Hawa wakaguzi ndio hutoa taswira ya namna ya fedha iliyoidhinishwa na kutolewa na Serikali kama imefika kwenye miradi au taasisi na pia wanaangalia kama fedha hizo zimetumika kwa usahihi," alisema Naibu Waziri Luswetula.

Alibainisha kuwa jukumu mojawapo la wakaguzi hao ni kuwa tayari kuhakikisha kwamba wanachunguza na kutoa majawabu sahihi kwa maana ya kutomuonea wala kumpendelea mtu yeyote.

Aidha aliongeza kuwa Serikali ipo tayari kuwaunga mkono wakaguzi katika kazi zao kuhakikisha wanafanyakazi katika mazingira yenye uhuru na yasiyo na vitisho na endapo patatokea muingiliano kwenye majukumu yao wawe huru kutoa taarifa hiyo mapema ili ufumbuzi upatikane.

Naye Rais na Mwenyekiti wa Bodi ya Taasisi ya Ukaguzi wa Ndani, Bw. Jonathan Ngoma akizungumza katika mkutano huo aliainisha kukosekana kwa uhuru kwa baadhi ya wakaguzi ndiko kunakosababisha kuendelea kwa mapungufu ya kiutendaji katika kaguzi kadhaa zinazofanyika maeneo mbalimbali.

"Mkaguzi yeyote anatakiwa awe huru aseme hapa kuna matatizo lakini sasa usipokuwa huru hutaweza kuyasema matatizo unayoyaona na ndio maana tumekuwa na matatizo ambayo hayaishi,...mwingine anayaona halafu wewe huyaoni na wakati mwingine hata akiyaona ataambiwa liache kama lilivyo, matokeo yake tunaishia mahali ambapo matatizo yataendelea kuwepo," alisema Bw. Ngoma.

Naye Msajili wa Hazina Zanzibar Waheed Muhammad Ibrahim amesema mafunzo hayo yanawajengea uwezo wa kuzitambua mbinu za ukaguzi zitakazowasaidia kwenye kazi zao za ukaguzi, huku Mkaguzi Mkuu wa Ndani Soko la hisa la Dar es salaam, Bw. Mecklaud Edson akisisitiza wakaguzi wa ndani kuwa macho ya serikali katika matumizi ya fedha kwa mashirika ya umma na miradi ya maendeleo.

Hata hivyo, alisema masuala ya kiutawala yanapaswa kupewa kipaumbele na kuwekewa mkazo katika taasisi za umma hasa zile zinazohusika katika masuala ya uwekezaji moja kwa moja pamoja na zenye bodi za wakurugenzi ili kuleta chachu na hatimaye kufikia malengo ya taasisi.

Mkutano wa nne wa Taasisi ya Wakaguzi wa Ndani na sekta za umma umewakutanisha wakaguzi wa ndani kutoka Taasisi mbalimbali za umma kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, lengo likiwa ni kuwajengea uwezo na kuzisaidia kamati za ukaguzi za ndani kutenda kazi zao vyema na ufanisi, kuweza kuhoji utawala kuhoji wakaguzi wa ndani na vitengo vya ukaguzi ili kuboresha huduma kwa wateja na watanzania wanaohitaji huduma.






Top News