-Awatoa hofu Watanzania wanaohofia upungufu wa dawa kutokana na mzozo mashariki ya kati

Na Said Mwishehe,Michuzi TV

MKURUGENZI Mkuu wa Bohari ya Dawa(MSD) Mavere Tukai amewahakikishia Watanzania kuwa upatikanaji wa dawa na vifaa tiba nchini uko imara kwani kuna akiba ya kutosha kwa kipindi cha zaidi ya miezi sita, licha ya kuendelea kwa mzozo wa Mashariki ya Kati.

Mkurugenzi Mkuu wa MSD, Mavere Tukai, ameyasema hayo katika kikao kazi kilichohusisha wahariri na waandishi wa habari walipokutana kujadili masuala mbalimbali katika sekta ya afya na hasa mchango wa MSD katika kuendeleza jitihada za kuhakikisha upatikanaji wa dawa na vifaa tiba unakuwa wa uhakika nchini.

Hivyo ametumia kikao hicho kuwatoa wasiwasi miongoni mwa wananchi kuhusu uwezekano wa kupungua kwa dawa na vifaa tiba, hasa kutokana na athari zinazoweza kusababishwa na mvutano wa kijeshi kati ya Marekani na Iran.

“MSD imejipanga vyema kuhakikisha upatikanaji endelevu wa bidhaa hizo muhimu na tayari kuna tathmini inayoendelea kufanywa na timu maalumu ya wataalamu ili kubaini hatari zinazoweza kujitokeza na kuweka mikakati madhubuti ya kukabiliana nazo.”

Mkurugenzi Mkuu ameongeza juhudi zinaendelea kuimarishwa, hasa katika kuhakikisha upatikanaji wa dawa na vifaa tiba vinavyoagizwa kutoka nje ya nchi hauathiriki na mabadiliko ya hali ya usalama na uchumi wa kimataifa.

“Serikali itaendelea kufuatilia kwa karibu mwenendo wa hali hiyo ili kuhakikisha huduma za afya nchini haziathiriki na wananchi wanaendelea kupata huduma bora bila usumbufu.









Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ameongoza kikao cha Kamati ya Pamoja ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (SJMT) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) ya kushughulikia Masuala ya Muungano kilichofanyika katika Ukumbi wa Golden Tulip Zanzibar.

Makamu wa Rais amewapongeza viongozi na wataalamu wote walioshiriki katika kikao hicho kwa jitihada walizofanya wakati wa maandalizi na majadiliano.

 Katika kikao hicho Hoja ya Uingizaji wa Sukari kutoka Zanzibar katika Soko la Tanzania Bara imeridhiwa na kuondolewa katika orodha ya Hoja za Muungano, ambapo imeshuhudiwa kusainiwa kwa Hati ya makubaliano ya kuondoa Hoja hiyo katika orodha ya Hoja za Muungano ambayo ni miongoni mwa hoja nne za Muungano zilizokuwa zimesalia. 

Kikao hicho kimehudhuriwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla, Waziri Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhandisi Hamad Masauni, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili ya Rais (Sera, Uratibu na Baraza la Wawakilishi) Mhe. Hamza Hassan Juma,Mawaziri na Manaibu Mawaziri wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Katibu Mkuu Kiongozi Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Balozi Dkt. Moses Kusiluka, Kaimu Katibu Mkuu Kiongozi Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Bw. Saleh Juma Mussa, Makatibu Wakuu, Wakuu wa Taasisi pamoja na Wataalamu mbalimbali.











 

Na Mwandishi Wetu

MAMLAKA ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imepokea vifaa vya kisasa vya uchunguzi wa kimaabara kutoka Ofisi ya Umoja wa Mataifa inayoshughulikia Dawa za Kulevya na Uhalifu (UNODC), ikiwa ni pongezi  baada ya kutambua mafanikio yaliyofikiwa na  Tanzania  katika udhibiti wa dawa za kulevya nchini.

Pongezi hizo zimetolewa jijini Dar es Salaam na ujumbe wa UNODC ukiongozwa na Mwakilishi wa  Kanda ya Afrika Mashariki, Ali El-Bereir, ambaye aliipongeza Tanzania kwa jitihada zinazofanyika katika kudhibiti biashara na matumizi ya dawa za kulevya pamoja na kemikali bashirifu.

Vifaa hivyo  hutokewa mahsusi kuzijengea uwezo taasisi zinazosimamia udhibiti wa dawa za kulevya katika ngazi ya kimataifa chini ya mpango wa Kimataifa wa Port Security and Safety of Navigation Programme (EU PSP). huo umetolewa chini ya mpango wa kimataifa wa Port Security and Safety of Navigation Programme (EU PSP) 

Vifaa vilivyotolewa ni pamoja na mashine za kisasa zenye uwezo wa kubaini kwa haraka aina mbalimbali za dawa za kulevya na kemikali zinazodhibitiwa hata zikiwa ndani ya vifungashio vyake bila kufunguliwa. Hivyo, kuwezesha ufanisi wa kichunguzi na kuboresha utendaji kazi wa Mamlaka. 

Aidha, UNODC imeahidi kuendelea kushirikiana na Tanzania kwa kutoa mafunzo na kuwajengea uwezo maafisa  wa DCEA Ili kuimarisha mapambano. 







Na. Edmund Salaho - Dodoma

Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) limeendelea kuimarisha safu yake ya Uongozi ili kuboresha utendaji kazi wa Shirika hilo kwa kuwaapisha na kuwavisha vyeo Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi (1) Makamishna Wasaidizi wa Uhifadhi (3) pamoja na Afisa Uhifadhi Mkuu (1) zoezi ambalo limefanyika leo Aprili 25, 2026 katika Ofisi Kiunganishi za TANAPA jijini, Dodoma.

Akizungumza katika hafla hiyo ya kuwavisha vyeo Makamishna hao Kamishna wa Uhifadhi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) Musa Nassoro Kuji,alitoa msisitizo kwa Makamishna hao kufanya Kazi kwa bidii, weledi na kusikiliza watu wanaowaongoza ili kuleta tija zaidi pamoja na kufikia malengo ya Shirika na Taifa kwa ujumla.

"Nendeni mkachape kazi kwa bidii na weledi huku mkiishi viapo vyenu mlivyoapa leo. Kiongozi mzuri ni yule anaesikiliza mawazo ya watu wake anaowaongoza hivyo, mkasikilize watu mnaowaongoza" alisisitiza Kamishna Kuji.

Akitoa shukurani kwa niaba ya Makamishna wapya, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi, Abdallah Omary Kiwango alishukuru Bodi ya Wadhamini TANAPA pamoja na Uongozi wa Shirika kwa imani kubwa walionayo juu yao.

"Napenda kuchukua nafasi hii kwa niaba ya Makamishna wenzangu  kuishukuru Bodi ya Wadhamini na Uongozi wa Shirika kwa kutuamini na kutukabidhi majukumu haya kama tulivyotoka kuapa, tunaahidi kufanya kazi kwa bidii na weledi wa hali ya juu ili kufanikisha malengo ya Taasisi ya kuendeleza Uhifadhi endelevu na kukuza Utalii katika Hifadhi za Taifa"

"Leo sio mwisho wa safari bali ni mwanzo wa dhamira mpya. Tunachukua majukumu haya tukiwa na nia thabiti ya kufanya kazi kwa weledi, nidhamu na uadilifu wa hali ya juu. Tuko tayari kujitoa kwa nguvu zote kuhakikisha tunalinda rasilimali za Taifa letu kwa faida ya kizazi cha sasa na kijacho" alisema Kamishna Kiwango

Makamishna wa Uhifadhi walioapishwa leo ni Abdallah Omary Kiwango ambaye ameapishwa kuwa Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi, Makamishna Wasaidizi wa Uhifadhi, Philbert  Michael Ngoti, Joachim Shaaban Tesha, Michael Joseph Tarimo pamoja na Afisa Uhifadhi Mkuu, Manendo Peter Maziku.







Na Janeth Raphael MichuziTv 


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amesema uzinduzi wa meli ya kwanza ya uvuvi wa bahari kuu ya Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO) ni hatua muhimu inayoweka msingi imara wa utekelezaji wa sera na mikakati ya nchi katika kuendeleza sekta ya uvuvi na kukuza uchumi wa buluu.

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya uzinduzi wa meli hiyo, Rais Samia alisema hatua hiyo ni sehemu ya mabadiliko ya kimkakati katika usimamizi na udhibiti wa rasilimali za bahari kuu, huku ikilenga kuongeza mchango wa sekta ya uvuvi katika uchumi wa taifa.

Rais Samia amesema Serikali imejidhatiti kulifufua na kuliimarisha Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO) ili liweze kushiriki kikamilifu katika kusimamia na kunufaika na rasilimali zilizopo katika bahari kuu kwa manufaa ya Watanzania wote.

Ameongeza kuwa uzinduzi wa meli hiyo unaakisi maono mapya ya Serikali katika kuhakikisha rasilimali za bahari zinasimamiwa kwa tija, uwazi na ufanisi zaidi, ili kuongeza mapato ya taifa na ajira kwa wananchi.

Katika hotuba yake, Rais Samia pia amesisitiza dhamira ya Serikali ya kuendelea kuimarisha taasisi nyingine za udhibiti na usimamizi wa rasilimali za uvuvi ili kukabiliana na changamoto ya uvuvi haramu unaoharibu mazingira na kuhatarisha uhai wa viumbe vya majini.

Amesema Serikali itaendelea kuchukua hatua madhubuti za kukomesha uvuvi usiozingatia sheria na taratibu, ili kuhakikisha uendelevu wa rasilimali za bahari kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

Aidha, Rais Samia amesema Serikali imefanya jitihada kubwa kuboresha mazingira ya shughuli za uvuvi katika maziwa na bahari kwa kuwezesha upatikanaji wa mitaji, utaalamu na vifaa, ikiwemo boti za kisasa za uvuvi pamoja na kuendeleza teknolojia za ufugaji samaki kwa njia ya vizimba.

Uzinduzi wa meli hiyo ya kwanza ya uvuvi wa bahari kuu kwa TAFICO unatajwa kuwa hatua muhimu katika kuimarisha sekta ya uvuvi nchini na kuongeza uwezo wa Tanzania kunufaika na uchumi wa buluu kupitia rasilimali zake za baharini.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akibonyeza Kitufe kuashiria Uzinduzi wa Meli ya Kwanza ya Uvuvi wa Bahari Kuu kwenye hafla fupi iliyofanyika katika Makao Makuu ya Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO) Kigamboni Jijini Dar es Salaam tarehe 25 Aprili, 2026.





 

-Pia mapato yaongezeka yafikia bilioni 640.5 katika kipindi cha miaka minne

Na Said Mwishehe,Michuzi TV-Dodoma

BOHARI ya Dawa(MSD) ambayo ni taasisi iliyoundwa kisheria mwaka 1993 ikifuatiwa na maboresho mbalimbali ya sheria ili kuiwezesha kutekeleza majukumu yake ya msingi imeendelea kujivunia mafanikio yaliyopatikana katika utoaji huduma za afya nchini.

Akizungumza leo Aprili 24,2026 wakati wa kikao kazi kilichoandaliwa na MSD na kuhusisha Wahariri na waandishi wa habari Mfamasia kutoka kitlendi cha Mipango,Ufuatiliaji na Tathimini Lilian Magesa kutoka MSD ametumia nafasi hiyo kuelezea kuwa kumekuwepo na mafanikio katika kipindi cha miaka minne 2021/22 hadi mwaka 2024/25.

Amefafanua katika kipindi cha miaka minne mapato ya MSD yameongezeka kwa asilimia 103 kutoka Sh.Bilioni 315.12 hadi kufikia kiasi cha Sh.Bilioni 640,5 mwaka 2024/25.

Pia mafanikio mengine ni kuongezeka kwa upatikanaji wa bidhaa za afya ashiri kutoka asilimia 42 mwaka 2021/22
hadi kufika asilimia 73 Machi, 2026.


“Hali ya utimizaji wa mahitaji wa vituo vya kutolea huduma za afya umeendelea kuongezeka kutoka asilimia 4l hadi kufikia asilimia 77 katika kipindi cha miaka minne.”

Pia amesema mafanikio mengine ni kuongezeka kwa mizunguko ya usambazaji wa bidhaa za afya kwenda vituo vya kutolea
huduma za afya kutoka mizunguko minne kwenda mizunguko sita kwa mwaka huku ununuzi wa bidhaa za kuwezesha uzazi pingamizi ( CEmONO) umefikia asilimia 100 ya
MS.

Ameongeza kuwa mafanikio mengine mashine 162 za kusafisha damu(dialysis) zimesambazwa kutoka mashine 60 mwaka 2021/2022 zilizogharimu Sh.bilioni 10.14

Pia kukamilisha ujenzi wa maghala ya kisasa yanayokidhi viwango vya uhifadhi na kuanza kutumika katika Kanda ya Dodoma na Mtwara -mita za mraba 12,000.Aidha kuanza kwa ujenzi wa ghala la Chato mkoani Geita lilifikia asilimia 42 ya utekelezaji.

Mafanikio mengine ni uanzishwaji wa kampuni tanzu ijulikanayo kama MSD Medipharm Manufacturing Company yenye jukumu la kusimamia uzalishaji unaotekelezwa kibiqshara na kwa ufanisi mkubwa .

“Pia kiwanda cha mipira ya mikono -Idofi kukamilika na kuanza kazi rasmi ya uzalishaji Februari 2024 pamoja na ongezeko la thamani ya bidhaa zinazonunuliwa kutoka kwa wazalishaji wa ndani kutoka Sh.bilioni 15.90 zilizonunuliwa mwaka 2021/22 hadi Sh.bilioni 98.72 mwaka 20/2024/25, ”amesema. 

Kuhusu changamoto amesema mojawapo ni uhaba wa mtaji wa kuwezesha;Ununuzi wa bidhaa za Afya toshelevu kwa kiwango cha miezi 5, Ujenzi wa miundombinu toshelezi na inayokidhi viwango vya uhifadhi pamoja na ushiriki na uanzishai wa viwanda vya bidhaa za afya.

Pia uwepo wa madeni, Washitiri kuchelewa kuleta bidhaa za afya kulingana na mikataba,ufinyu wa maeneo ya kuhifadhia bidhaa za Afya licha ya kuongezeka kwa idadi ya watu na mahitail na utegemezi wa uagizaji kutoka nje ya nchi kutokana na uwezo hafifu wa viwanda vya ndani.








Serikali kupitia Tume ya Madini imesema itaendelea kutoa bei elekezi za madini ya dhahabu, shaba na fedha kila siku itakayotumika kwenye masoko na vituo vya ununuzi wa madini hatua inayolenga kuongeza uwazi katika biashara ya madini na kuwawezesha wachimbaji kuuza madini yao kwa bei halisi ya soko la dunia.

Akifunga mafunzo kwa Mameneja na Wakaguzi Wakuu wa Migodi ya uchimbaji mdogo kutoka mikoa ya kimadini ya Kahama, Mbogwe na Shinyanga mapema jana, Mkurugenzi wa Ukaguzi na Biashara ya Madini, CPA Venance Kasiki alisema taarifa hizo za bei zitawasaidia wachimbaji kufanya maamuzi sahihi ya biashara na kuepuka hasara zitokanazo na madalali maarufu kama vishoka.

Alisema hapo awali baadhi ya wachimbaji walikuwa wakiuza madini bila kufahamu bei halisi ya soko la dunia, hali iliyosababisha kupoteza mapato na kuingia katika mikataba isiyo na manufaa.

Alifafanua kuwa kwa sasa bei za madini hutolewa kila siku, hivyo mchimbaji ana uwezo wa kufanya uamuzi sahihi kabla ya kuuza madini yake.

Aidha, alisema Serikali inaendelea kuimarisha mifumo ya uwazi katika biashara ya madini pamoja na kuwahamasisha wananchi kutoa taarifa za vitendo vya utoroshaji wa madini, ambapo watoa taarifa watapatiwa zawadi maalum.

CPA Kasiki alionya kuwa watakaobainika kujihusisha na utoroshaji wa madini watakabiliwa na hatua kali za kisheria ikiwemo kufunguliwa mashitaka, kutaifishwa madini, kulipa faini pamoja na kifungo kwa mujibu wa sheria.

Katika hatua nyingine, alisisitiza umuhimu wa kuzingatia usalama migodini, akibainisha kuwa uchimbaji usiofuata taratibu hauwezi kuwa endelevu, huku akisisitiza kuwa uhai wa binadamu una thamani kubwa kuliko madini.

Aliwahimiza wachimbaji kutumia maabara ya Tume ya Madini katika kupima sampuli ili kufanya maamuzi sahihi badala ya kutumia maabara zisizotambulika.

Aidha, aliwakumbusha wamiliki wa leseni kufanya miradi endelevu kwa jamii zinazozunguka migodi ikiwa ni utekelezaji wa takwa la Kisheria la wajibu wa mwenye leseni kwa jamii (CSR).

Awali, Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Migodi na Mazingira, Mhandisi Hamisi Kamando alisema mwitikio wa washiriki ulikuwa mkubwa ambapo kati ya washiriki 400 waliotarajiwa, washiriki 370 walijitokeza, jambo linaloonesha hamasa kubwa ya wachimbaji kujifunza masuala ya usalama, afya na utunzaji wa mazingira.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa SHIREMA, Hamza Tandiko alisema mafunzo hayo yameongeza uelewa wa wachimbaji katika biashara ya madini, matumizi salama ya kemikali na baruti, uhifadhi wa mazingira pamoja na uchunguzi wa ajali migodini, akisisitiza umuhimu wa kuachana na uchimbaji wa kubahatisha na kuingia katika uchimbaji wa kisasa na wenye tija.




 

Na Augusta Njoji

Timu ya wataalamu wa afya kutoka Hospitali ya Halmashauri ya Mji Handeni imeanza rasmi mpango wa utoaji elimu kwa jamii ili kuimarisha kinga dhidi ya magonjwa na kuboresha ustawi wa wananchi.

Utoaji wa elimu hiyo imejikita katika afua za kuzuia malaria, lishe bora, bima ya afya kwa wote pamoja na huduma za mama na mtoto, ikiwa ni sehemu ya jitihada za serikali kuhakikisha jamii inakuwa na afya bora.

Akizungumza kuhusu zoezi hilo, Ofisa Afya wa Halmashauri na Mratibu wa Elimu ya Afya kwa Umma, Jonas Mkondya, amesema wamejipanga kutembelea kila mtaa katika kata zote 12 za Halmashauri ya Mji Handeni ili kuwafikia wananchi wengi zaidi na kuwapatia elimu sahihi ya afya.

Ameeleza kuwa elimu hiyo itasaidia kuongeza uelewa kwa wananchi juu ya namna ya kujikinga na magonjwa, kuboresha lishe pamoja na umuhimu wa kujiunga na bima ya afya kwa wote ili kupata huduma kwa urahisi.

Kata zitakazofikiwa katika ziara hiyo ya wataalamu wa afya ni Konje, Mabanda, Kwenjugo, Malezi, Chanika, Mlimani, Mdoe, Vibaoni, Kwediyamba, Kideleko, Msasa na Kwamagome.


Top News