Meneja wa Kanda Namba Sita, Halmashauri ya Jiji la Dodoma Lucas Nkelege amekutana na watendaji wa kata pamoja na watendaji wa mitaa inayounda kanda hiyo kwa lengo la kutoa elimu ya vyanzo vya mapato na kuwakumbusha umuhimu wa ukusanyaji wa mapato kwa wakati ili kuongeza ufanisi wa huduma kwa wananchi.

Akizungumza katika kikao hicho, Nkelege ameeleza kuwa mapato yanayokusanywa katika maeneo mbalimbali ndiyo msingi wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo pamoja na kuboresha huduma muhimu za jamii ikiwemo usafi wa mazingira, ujenzi wa miundombinu na huduma za kijamii.

Amesisitiza kuwa watendaji wanapaswa kuwa mstari wa mbele katika kutoa elimu kwa wananchi kuhusu ulipaji wa tozo na ada mbalimbali kwa hiari na kwa kuzingatia taratibu zilizowekwa, huku akiongeza kuwa ukusanyaji wa mapato ni jukumu la pamoja linalohitaji ushirikiano wa karibu kati ya watendaji wa kata, mitaa na viongozi wa serikali za mitaa. 

“Ukusanyaji wa mapato si kazi ya mtu mmoja, ni jukumu la pamoja. Tukishirikiana kwa karibu, tutakusanya mapato kwa ufanisi na kuleta maendeleo ya haraka kwa wananchi wetu” alisema Nkelege.

Watendaji wanahimizwa kutambua na kusimamia vyanzo vyote vya mapato vilivyopo kwenye maeneo yao ikiwemo biashara ndogondogo, ushuru wa huduma, ada za vibali na vyanzo vingine halali vya mapato ili kuzuia upotevu wa mapato.







Nimezungumza na maafisa tawala na RasilimaliWatu , katika mkutano uliofanyika Ukumbi wa AICC, Arusha na kuwakumbusha kutekeleza wajibu wao na kuleta furaha kwa watumishi wa umma ili kwa upande mwengine nao wapeleke furaha na neema kwa Watanzania . Nimeyaeleza hayo kufuatia maamuzi mbalimbali yanayofanywa na serikali ya awamu ya sita katika kuhakikisha maslahi ya Watumishi wa umma nchini yanaboreka.

Uamuzi wa hivi karibuni wa Serikali kupandisha madaraja watumishi 219,042 ni hatua ya kihistoria katika kuimarisha utumishi wa umma nchini Tanzania. Hatua hii ambayo imepata ridhaa ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na ongezeko la mishahara ya watumishi wa umma (2025): +35.1% , Ongezeko la kima cha chini sekta binafsi (2025/26): +33.4% , ambapo Sekta mbalimbali zinakwenda athiriwa na maboresho haya ikiwemo afya, elimu, kilimo, mawasiliano, usafirishaji, nishati, viwanda, biashara, hoteli, michezo, uvuvi, baharini, madini ,utamaduni n.k

Matokeo haya kitakwimu zinaonyesha kasi ya mageuzi ya kiutumishi chini ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan ambayo inaonyesha uongozi wa kimkakati unaoweka mbele ustawi wa watumishi na ufanisi wa taasisi za umma.





📍 Apandisha mishahara kwa asilimia 35


Na Mwandishi Wetu, Arusha

SERIKALI ya Awamu ya Sita imefanya mageuzi makubwa ya kiutumishi nchini kwa kupandisha madaraja watumishi wa umma 219,042, huku ikiongeza mishahara kwa asilimia 35.1, hatua inayotajwa kuwa ni kielelezo cha uongozi unaoweka mbele ustawi wa mfanyakazi.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete, ameyabainisha hayo leo jijini Arusha wakati akizungumza na Maafisa Tawala na Rasilimali Watu katika mkutano uliofanyika Ukumbi wa AICC.

Mhe. Kikwete alisema maamuzi hayo ya kimkakati yaliyopata ridhaa ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, yanalenga kuleta "furaha na neema" kwa watumishi wa umma ili nao waweze kutoa huduma bora na kupeleka furaha kwa Watanzania wote kupitia utendaji wao.

Ongezeko la Mishahara na Sekta Binafsi

Akifafanua kuhusu neema hiyo ya kiutumishi, Waziri Kikwete alibainisha kuwa mbali na ongezeko la 35.1% kwa watumishi wa umma mwaka 2025, Serikali pia imeimarisha sekta binafsi kwa kuongeza kima cha chini cha mishahara kwa 33.4% kwa mwaka wa fedha 2025/26.

Alisema maboresho hayo yanagusa sekta mbalimbali za kimkakati nchini ikiwemo Afya, Elimu, Kilimo, Mawasiliano, Usafirishaji, Nishati, Viwanda, Biashara, Madini, na Utalii.

"Nimezungumza na maafisa rasilimali watu na kuwakumbusha kutekeleza wajibu wao wa kuleta furaha kwa watumishi. Uamuzi wa Rais Samia kupandisha madaraja watumishi zaidi ya laki mbili ni hatua ya kihistoria katika kuimarisha utumishi wa umma nchini Tanzania," alisema Waziri Kikwete.

Waziri Kikwete aliongeza kuwa takwimu hizo zinaonyesha kasi ya mageuzi chini ya uongozi wa Rais Samia, ambaye amedhihirisha kwa vitendo kuwa ufanisi wa taasisi za umma unategemea sana kuimarika kwa maslahi na hali ya maisha ya watumishi.

Aliwataka Maafisa Tawala nchini kuhakikisha wanatekeleza maelekezo ya Serikali kwa uadilifu ili watumishi wapate haki zao kwa wakati, jambo litakaloongeza morali ya kazi na tija katika kuwahudumia wananchi.





Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na shirika la kimataifa la Brooke East Africa, inatarajia kuhitimisha kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Punda Kitaifa hapo kesho.

Hafla hiyo ya kimkakati imepangwa kufanyika katika Kata ya Mgusu, iliyopo ndani ya Halmashauri ya Manispaa ya Geita, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kitaifa za kutambua mchango wa mnyama huyu katika uchumi.

Uamuzi wa kuifanya Kata ya Mgusu kuwa kitovu cha maadhimisho haya umechangiwa na takwimu za kijiografia na kiuchumi zinazoonyesha mwingiliano mkubwa kati ya jamii na punda.

Afisa Mifugo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bi. Tabitha Kitingu, amebainisha kuwa eneo hilo lina idadi kubwa ya punda ambao ni kiungo muhimu katika mnyororo wa uzalishaji, hususan kwenye shughuli za uchimbaji madini.

Kwa mujibu wa tathmini za kitaalamu, Kata ya Mgusu pekee inakadiriwa kuwa na idadi inayozidi Punda 500.

Kutokana na idadi hiyo kubwa, Serikali imeona umuhimu wa kutoa kipaumbele katika utoaji wa elimu ya kina kwa wamiliki na watumiaji wa wanyama hao, lengo likiwa ni kuhakikisha punda wanapata huduma bora na stahiki kulingana na miongozo ya ustawi wa wanyama duniani.

Msingi mkuu wa maadhimisho haya ni kusisitiza haki za msingi za mnyama kazi, ambazo mara nyingi hupuuzwa kutokana na shinikizo la shughuli za kiuchumi migodini.

Elimu itakayotolewa inalenga kubadilisha mitazamo ya wafugaji ili wajali afya, lishe, na mapumziko ya punda, jambo ambalo ni muhimu katika kuongeza tija na uendelevu wa nguvu kazi ya mnyama huyo.

Kwa upande wake, Daktari wa Mifugo kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Geita, Dkt. David Misonge, amethibitisha kuwa wataalamu wa afya ya wanyama wamekusanywa kutoka maeneo mbalimbali mkoani humo.

Kikosi hicho cha wataalamu kimejipanga kutoa huduma za kitabibu na ushauri wa kitaalamu, hasa katika maeneo ya migodi ambapo punda hukabiliwa na changamoto nyingi za kiafya kutokana na kubeba mizigo mizito.

Maadhimisho haya pia yanajumuisha zoezi la uchunguzi wa afya na matibabu ya punda wenye magonjwa na majeraha mbalimbali yanayotokana na mazingira yao ya kazi.

Hatua hii ni sehemu ya mkakati mpana wa Serikali mkoani Geita wa kudhibiti maradhi ya mlipuko miongoni mwa mifugo na kuhakikisha kuwa mnyama kazi hapati mateso yasiyo ya lazima wakati wa utekelezaji wa majukumu yake.

Aidha, Serikali imesisitiza dhamira yake ya dhati ya kuendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo katika kutoa elimu endelevu kwa wananchi.

Lengo ni kujenga jamii yenye uelewa wa kisheria na kimaadili kuhusu utunzaji wa wanyama, ili kuondoa kabisa vitendo vya ukatili na kuhakikisha punda wanatibiwa kwa wakati wanapougua.

Kwa upande mwingine, jamii ya wafugaji na wakazi wa Geita wametoa shukrani zao za dhati kwa mashirika ya Brooke East Africa na ASPRA kwa mchango wao thabiti.

Mashirika haya yamekuwa mstari wa mbele katika kutoa matibabu ya ruzuku na mafunzo ya mbinu bora za ufugaji, hali inayochochea mabadiliko chanya ya kijamii na kiuchumi katika mkoa wa Geita.





Serikali itaendelea kuimarisha usimamizi na maendeleo ya taaluma ya ualimu nchini kupitia utekelezaji wa majukumu ya Bodi ya Kitaalamu ya Walimu Tanzania (Tanzania Teachers Professional Board), ikiwa ni sehemu ya juhudi za kulinda na kuinua hadhi ya taaluma hiyo.

Kupitia hatua hiyo, Serikali itaandaa mwongozo wa viwango vya ufundishaji ili kukuza mafunzo endelevu kwa walimu, pamoja na kuandaa Mwongozo wa Maadili na Mwenendo wa Taaluma ya Ualimu utakaosaidia kuimarisha nidhamu na weledi katika sekta ya elimu.

Hayo yameelezwa bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara yake kwa mwaka wa fedha 2026/27.

Katika hatua nyingine, Serikali itaanza kutekeleza mpango wa mafunzo kwa vitendo wa mwaka mmoja (internship) kwa wahitimu wa mafunzo ya ualimu, hatua inayolenga kuwawezesha walimu tarajali kuoanisha maarifa ya nadharia na uhalisia wa kazi darasani.

Aidha, Serikali itaendelea kuwajengea uwezo walimu wa shule za msingi na sekondari, wakufunzi wa vyuo vya ualimu, wathibiti ubora wa shule na wasimamizi wa elimu ili kuboresha utendaji katika sekta ya elimu.

Katika mpango huo, walimu 1,223 watanufaika na ufadhili wa masomo ya Stashahada ya Ualimu wa Elimu Maalum, huku walimu 3,000 wakipatiwa mafunzo ya ushauri na unasihi kuhusu malezi, stadi za maisha na ulinzi wa mtoto.

Vilevile, watendaji 5,500 pamoja na walimu na wanafunzi watanufaika na mafunzo kuhusu matumizi ya majukwaa ya kielimu, ikiwemo maktaba mtandao na majukwaa ya kujifunza mtandaoni kwa lengo la kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika elimu.



WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa Kikao Kazi cha 21 cha Maafisa Habari, Mawasiliano, Itifaki na Uhusiano Serikalini Mei leo 7, 2026 mkoani Njombe.

Kikao kazi hicho cha mwaka, kinawakutanisha zaidi ya Maafisa Habari 300 kutoka taasisi mbalimbali za Serikali kote nchini kwa lengo la kuwanoa na kuwajengea uwezo, kusimamia na kuzifikisha kwa ufanisi taarifa za Serikali kwa umma.

Kupitia kikaokazi hicho washiriki watapata mafunzo na kufanya mijadala mizito ikiwemo ya uandishi wa kisasa wa taarifa kwa umma, mbinu za kuandika makala zenye mvuto magazetini pamoja na kanuni muhimu za itifaki katika shughuli za kitaifa.

Aidha, watapata fursa ya kujifunza kuhusu matumizi sahihi ya picha za viongozi, utaratibu wa utajo rasmi na suala la mwonekano wa mavazi katika mikutano ya kitaifa na kimataifa

Katika hatua ya kuimarisha mawasiliano ya Serikali hadi ngazi za chini, washiriki wameendelea kuhimizwa kushirikiana kwa karibu na redio za kijamii pamoja na klabu za waandishi wa habari mikoani ili kuongeza ufanisi wa utoaji wa taarifa kwa wananchi.

Sambamba na kikao hicho, wananchi wa Mkoa wa Njombe wananufaika na huduma za kibingwa bobezi zinazotolewa na wataalamu kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili (Upanga na Mloganzila) pamoja na Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Ubongo Muhimbili (MOI).

Mbali na mafunzo hayo, washiriki pia watapata fursa ya kutembelea kiwanda cha AVO AFRICA kinachozalisha mafuta ya parachichi, kushuhudia vivutio vya asili ikiwemo maporomoko ya maji ya Mpanga Kipengele, na kushiriki zoezi la upandaji miti kulinda vyanzo vya maji katika Halmashauri ya Mji wa Njombe.

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan aongoza Kikao cha kawaida cha Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kilichoketi mkoani Dodoma tarehe 07 Mei 2026.

 

Na Mwandishi Wetu, Nairobi

Rais wa Kenya, William Ruto, amempongeza Jaji Mohammed Abdullahi Warsame baada ya kuapishwa rasmi kuwa jaji wa 14 wa Mahakama ya Juu ya Kenya, akieleza kuwa uzoefu wake mkubwa utasaidia kuimarisha utoaji wa haki nchini humo.

Akizungumza katika hafla iliyofanyika Ikulu ya Nairobi, Rais Ruto alisema ana imani kuwa Jaji Warsame ataleta mchango chanya katika mahakama hiyo ya juu kabisa nchini Kenya kupitia weledi na uzoefu wake wa muda mrefu katika sekta ya sheria.


 “Unaungwa mkono kikamilifu na tunakuombea mafanikio unapoanza jukumu hili muhimu la kulitumikia taifa letu,” alisema Ruto wakati wa hafla ya kuapishwa kwa jaji huyo.

Katika hafla hiyo pia, Rais Ruto aliwapongeza Evans Thiga Gaturu na Jedidah Wakonyo Waruhiu baada ya kutunukiwa hadhi ya Senior Counsel, akisema wameonyesha mchango mkubwa katika kuimarisha utawala wa sheria na demokrasia ya kikatiba nchini Kenya.

Ruto alisema Serikali ya Kenya itaendelea kushirikiana na mihimili mingine ya dola kuhakikisha haki inatendeka na mfumo wa sheria unaendelea kuimarika kwa manufaa ya wananchi wote.

Hafla hiyo ilihudhuriwa pia na Naibu Rais wa Kenya, Kithure Kindiki pamoja na Jaji Mkuu na Rais wa Mahakama ya Juu Kenya, Martha Koome.







Uongozi wa Taasisi ya LALJI FOUNDATION ukiwa katika picha ya pamoja na wanachama wa Chama cha Wanawake Wajane Tanzania (CCWWT) mkoani Kigoma mara baada ya kukabidhi mizinga 50 ya nyuki, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuwawezesha wajane kiuchumi kupitia ufugaji nyuki.

KATIKA juhudi za kuwawezesha wanawake wajane kujikwamua kiuchumi, Taasisi ya LALJI FOUNDATION imekabidhi mizinga 50 ya nyuki kwa Chama cha Wanawake Wajane Tanzania (CCWWT) mkoani Kigoma, ikiwa ni sehemu ya mpango wa kukuza kipato kupitia ufugaji nyuki.

Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano hayo, Katibu wa LALJI FOUNDATION, Bi. Fatema Imtiaz Lalji, amesema kuwa huo ni mwanzo wa utekelezaji wa mpango mkubwa unaolenga kugawa jumla ya mizinga 200 kwa wajane katika maeneo mbalimbali nchini.

Amesema taasisi hiyo imeanza na mkoa wa Kigoma kwa kuwalenga wajane, ambao mara nyingi hukumbana na changamoto za kiuchumi na kijamii, hivyo kuwapatia fursa ya kujipatia kipato kupitia ufugaji nyuki.

“Tunatambua mchango wa wanawake katika jamii, lakini pia tunatambua changamoto wanazokutana nazo, hususan wajane. Kupitia mradi huu, tunalenga kuwapa uwezo wa kujitegemea kiuchumi,” amesema Bi. Lalji.

Ameongeza kuwa zoezi hilo litakuwa endelevu, huku taasisi hiyo ikiendelea kufikia makundi mbalimbali yenye uhitaji katika maeneo tofauti nchini.

Amesema Kabla ya kukabidhi mizinga hiyo LAJI FOUNDATION iliendesha mafunzo ya kitaalamu kwa wanufaika wa mradi huo ambayo yalifanyika Febuari 15, 2026 Wilayani Bagamoyo ili kuhakikisha wanapata ujuzi sahihi wa utunzaji wa mizinga, uvunaji wa asali kwa njia salama, pamoja na uhifadhi wa bidhaa zitokanazo na nyuki.

“Mafunzo hayo yatasaidia kuongeza tija na ubora wa mazao, hivyo kuwawezesha wajane hao kushindana katika soko”

Ameongeza kuwa pamoja na kugawa mizinga, pia kuna mpango wa kuwasaidia wanufaika kupata masoko ya uhakika ya bidhaa zao, ikiwemo asali na nta, ili kuhakikisha wanapata faida stahiki. Hatua hiyo inalenga kuondoa changamoto ya soko ambayo imekuwa ikiwakwamisha wafugaji wengi wadogo nchini.

Kwa upande wao, wanachama wa CCWWT mkoani Kigoma wameishukuru LALJI FOUNDATION kwa msaada huo, wakisema utasaidia kubadilisha maisha yao na kuongeza kipato cha familia.

Wamesema ufugaji nyuki ni fursa muhimu inayoweza kuleta maendeleo endapo watapatiwa elimu na usimamizi mzuri, huku wakiahidi kuitunza na kuitumia vizuri mizinga hiyo ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Mradi huo unatarajiwa kuwa chachu ya maendeleo kwa wajane hao, huku ukichangia pia katika uhifadhi wa mazingira na uzalishaji wa mazao ya nyuki kama asali, nta na bidhaa nyingine zitokanazo na nyuki
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (Katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Habib African, Bw. Faraz Haider (Kushoto) na Mwenyekiti wake wa Bodi wa Benki hiyo anayemaliza muda wake, Bw. Zain Habib (kulia), baada ya kikao chao kilichofanyika katika Ofisi Ndogo ya Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaaam, ambapo wamezungumza fursa mbalimbali zilizopo nchini hasa katika uwekezaji katika Nyumba za makazi za bei rahisi katika miji inayokuwa kwa kasi nchini.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (kulia) Akimkabidhi zawadi ya baadhi ya bidhaa za kilimo zinazozalishwa nchini, Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Habib African, Bw. Faraz Haider, baada ya kikao chao kilichofanyika katika Ofisi Ndogo ya Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaaam, ambapo wamezungumza fursa mbalimbali zilizopo nchini hasa katika uwekezaji katika Nyumba za makazi za bei rahisi katika miji inayokuwa kwa kasi nchini.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini,WF, Dar es Salaam)


Na Mwandishi wetu

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, ameliomba Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuidhinisha jumla ya Shilingi trilioni 2.39 kwa ajili ya utekelezaji wa bajeti ya Wizara ya Elimu kwa mwaka wa fedha 2026/2027, ikiwa ni hatua inayolenga kuimarisha maendeleo ya sekta ya elimu, sayansi na teknolojia nchini.

Akiwasilisha hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara hiyo Kwa mwaka wa fedha 2026/27 Bungeni jijini Dodoma, Prof. Mkenda amesema fedha hizo zitatumika kugharamia matumizi ya kawaida pamoja na utekelezaji wa miradi ya maendeleo yenye lengo la kuboresha ubora wa elimu nchini.

Kwa mujibu wa makadirio hayo, Wizara ya Elimu (Fungu 46) inaomba kuidhinishiwa jumla ya Shilingi 2,394,423,829,000, ambapo Shilingi 697,841,881,000 zimetengwa kwa ajili ya matumizi ya kawaida ya Wizara.

Kati ya fedha hizo za matumizi ya kawaida, Shilingi 648,082,352,000 zitatumika kulipa mishahara ya watumishi wa Wizara, huku Shilingi 49,759,529,000 zikitengwa kwa ajili ya matumizi mengineyo ya uendeshaji wa shughuli za kila siku za Wizara.

Aidha, kwa upande wa miradi ya maendeleo, Wizara imeomba jumla ya Shilingi 1,696,581,948,000, ambapo kati ya hizo Shilingi 1,337,249,000,000 ni fedha za ndani na Shilingi 359,332,948,000 ni fedha kutoka kwa washirika wa maendeleo.

Vilevile, kupitia Tume ya Taifa ya UNESCO (Fungu 18), Wizara imeomba kuidhinishiwa Shilingi 3,866,993,000 kwa ajili ya matumizi ya kawaida, ambapo Shilingi 1,335,020,000 zitatumika kwa mishahara na Shilingi 2,531,973,000 kwa matumizi mengineyo ya uendeshaji.

Kwa ujumla, Wizara ya Elimu na Tume ya UNESCO imeomba Bunge kuidhinisha jumla ya Shilingi 2,398,290,822,000 kwa ajili ya utekelezaji wa bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027.

Prof. Mkenda amehitimisha hotuba yake kwa kutoa shukrani kwa Spika wa Bunge, Waheshimiwa Wabunge na wadau wote kwa ushirikiano wao, akisisitiza kuwa bajeti hiyo itachochea kwa kiasi kikubwa maendeleo ya sekta ya elimu nchini na kuongeza ubora wa huduma za elimu kwa wananchi.


Na Mwandishi wetu Dodoma

Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Juma Homera, leo Mei 07, 2026 amekutana na wananchi wa eneo la Mtumba jijini Dodoma kupitia programu maalum ya “Sema na Waziri”  inayoratibiwa na Kituo cha Huduma kwa Mteja cha Wizara hiyo, kwa lengo la kusikiliza na kutatua changamoto mbalimbali za kisheria zinazowakabili wananchi.

Kupitia programu hiyo, wananchi walipata nafasi ya kuwasilisha kero zao moja kwa moja kwa Waziri, kupata ushauri wa kisheria pamoja na kuelekezwa namna sahihi ya kutatua migogoro mbalimbali inayohitaji msaada wa kisheria.

Akizungumza na wananchi hao, Dkt. Homera amesema serikali imejipanga kuhakikisha huduma za kisheria zinasogezwa karibu zaidi na wananchi ili kila Mtanzania aweze kupata haki kwa urahisi bila vikwazo vya kifedha au urasimu.

Amesema bado kuna wananchi wengi wasiokuwa na uwezo wa kugharamia kesi mahakamani au hata kufahamu namna ya kushughulikia changamoto zao za kisheria, hali inayosababisha baadhi yao kuendelea kuathirika bila msaada sahihi.

“Wapo wananchi ambao hawana uwezo wa kifedha wa kwenda mahakamani, lakini pia zipo changamoto ambazo zinahitaji ufafanuzi wa kisheria tu. Zikifika kwetu tunazifanyia kazi na kutoa mwongozo stahiki,” amesema Dkt. Homera.

Aidha, amesema Wizara ya Katiba na Sheria imeendelea kujiimarisha katika utoaji wa huduma kwa wananchi kwa kuhakikisha kila anayewasilisha changamoto yake anasikilizwa na kupata msaada unaohitajika kwa wakati.

“Sheria ni sehemu ya maisha yetu ya kila siku. Ndiyo maana kila mwananchi anayepiga simu au kufika kuwasilisha changamoto yake lazima asikilizwe. Mpaka sasa kupitia programu hii tayari tumeshatatua kero zaidi ya 100 za wananchi,” amesema.

Katika hatua nyingine, Dkt. Homera ametoa rai kwa Watanzania kujenga utamaduni wa kutatua migogoro kwa njia ya maridhiano badala ya kupeleka kila jambo mahakamani, akisema hatua hiyo itasaidia kupunguza msongamano wa mahabusu na wafungwa magerezani.

“Si kila kesi lazima iende mahakamani. Zingine zinaweza kutatuliwa ndani ya familia au kupitia maridhiano ya kijamii. Hii itasaidia kupunguza migogoro isiyo ya lazima pamoja na msongamano wa watu magerezani,” amesema.

Pia amebainisha kuwa miongoni mwa changamoto kubwa zinazowasilishwa mara kwa mara katika programu hiyo ni migogoro ya ardhi na mirathi, huku akisisitiza umuhimu wa wananchi kuandika usia mapema wakiwa hai ili kuepusha migogoro ya kifamilia baada ya vifo.

“Changamoto kubwa tunazokutana nazo ni masuala ya ardhi na mirathi. Niwasihi Watanzania kuandika usia mapema wakiwa hai ili kuepusha migogoro inayojitokeza baada ya ndugu kufariki,” amesema.

Programu ya “Sema na Waziri” imeendelea kuwa jukwaa muhimu la kuwafikia wananchi moja kwa moja, kusikiliza changamoto zao na kuwapatia msaada wa kisheria kwa lengo la kuimarisha upatikanaji wa haki nchini. 



KATIKA dunia ya sasa ya burudani ya mtandaoni, Meridianbet imekuja na kitu tofauti kabisa kinachoitwa Missions. Hii siyo tu kucheza kawaida, bali ni mfumo unaokupa uzoefu wa kipekee ambapo kila hatua unayochukua ina maana na inakupeleka mbele zaidi. Hapa burudani inakuwa safari ya kusisimua yenye malengo na mwelekeo.

Kitu kinachofanya Meridianbet Missions kuwa ya kipekee ni uhuru wako wa kuchagua. Wewe ndiye unaamua aina ya changamoto unazotaka kulingana na michezo unayoipenda. Hii inamaanisha kila mchezaji ana nafasi sawa ya kufurahia kwa njia yake binafsi na kufurahia.

Vilevile, Michezo mingi zaidi ya kubashiri inaendelea kupatikana ndani ya Meridianbet ikiwa na ODDS kubwa na machaguo mengi zaidi. Kushiriki ni vyepesi kupitia tovuti ya MERIDIANBET au kwa kupiga *149*10#.

Zaidi ya hapo, mfumo huu unakuonyesha maendeleo yako kwa uwazi kabisa. Unaweza kuona ulipoanzia, ulipo sasa, na unakoelekea. Hii inakupa motisha ya kuendelea kushiriki kwa mpangilio na nidhamu, huku ukifurahia kila hatua ya safari yako ndani ya jukwaa la Meridianbet.

Kadri unavyoendelea kushiriki na kukusanya pointi, ndivyo unavyopanda ngazi kama Bronze, Silver hadi Gold. Hii siyo tu ishara ya mafanikio, bali ni njia ya Meridianbet kuthamini juhudi na ushiriki wako wa muda mrefu. Kila ngazi inakupeleka kwenye uzoefu mpya na wa kuvutia zaidi.

Kwa ujumla, Meridianbet Missions ni zaidi ya burudani ya kawaida, ni mfumo unaochanganya mkakati, motisha na burudani kwa pamoja. Kwa vijana wanaopenda uzoefu wa kisasa wa kidijitali, hii ni nafasi ya kufurahia kwa njia mpya na ya kipekee ndani ya Meridianbet.


Na Janeth Raphael- MichuziTv -Dodoma

Serikali imesema inaendelea kuimarisha mfumo wa usuluhishi wa migogoro ya ndoa nchini ili kupunguza ucheleweshaji wa mashauri ya talaka na kusaidia wanandoa kupata suluhu kabla ya kufikishana mahakamani.

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Zainab Katimba, amesema hayo leo Mei 7, 2026 Bungeni jijini Dodoma alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu, Happiness Ngwando, aliyetaka kujua mpango wa Serikali wa kurekebisha Sheria ya Ndoa ili kuharakisha umalizaji wa kesi za talaka.

Mhe. Katimba amesema kifungu cha 9 cha Sheria ya Ndoa, Sura ya 29, kinaitafsiri ndoa kuwa ni muunganiko wa mwanamke na mwanaume kwa lengo la kuishi pamoja maisha yote, hivyo sheria hiyo imeweka utaratibu wa mashauri ya ndoa kuanza kusikilizwa katika Bodi za Usuluhishi wa Ndoa kabla ya kufikishwa mahakamani.

Amesema lengo la utaratibu huo ni kutoa nafasi ya maridhiano na kutafuta suluhu badala ya wanandoa kuachana haraka.

Aidha, amesema Mahakama ya Tanzania imeweka mwongozo maalumu wa muda wa usikilizaji wa kesi ili kuharakisha utoaji wa haki. Kwa mujibu wa mwongozo huo, mashauri katika Mahakama za Mwanzo yanapaswa kukamilika ndani ya miezi sita, Mahakama za Wilaya na Mahakama za Hakimu Mkazi ndani ya mwaka mmoja, huku Mahakama Kuu ikiwa na ukomo wa miaka miwili.

“Mashauri ya talaka pia yanaweza kusikilizwa na kuamuliwa katika Mahakama za Mwanzo kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizopo,” amesema Mhe. Katimba.

Katika hatua nyingine, amesema Serikali kupitia Wizara ya Katiba na Sheria imeanza programu ya kuwajengea uwezo wajumbe wa Bodi za Usuluhishi wa Ndoa nchi nzima ili kuongeza ufanisi katika utatuzi wa migogoro ya kifamilia.

Amesema utekelezaji wa programu hiyo ulianza rasmi Aprili 8, 2026 mkoani Kagera, ukiwa na lengo la kuhakikisha wanandoa wenye migogoro wanapata ushauri na suluhu stahiki kabla ya kufungua mashauri ya talaka mahakamani.



Top News