Jane Mwakyoma, July 15, 2026, Rukwa.

MKUU wa Mkoa wa Rukwa Charles Makongoro Nyerere ameipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi kwa kufanikiwa kupata hati safi akieleza kuwa mafanikio hayo ni kielelezo cha usimamizi bora wa fedha za umma na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu ya Serikali.

Nyerere ametoa pongezi wakati akizungumza katika Baraza Maalum la Madiwani la kujadili Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).

Amesema mafanikio hayo yametokana na ufungaji mzuri wa vitabu vya hesabu za Serikali, uzingatiaji wa sheria, kanuni na taratibu za matumizi ya fedha za umma, usimamizi madhubuti wa rasilimali, ukusanyaji mzuri wa mapato, utekelezaji wa bajeti kwa ufanisi, pamoja na ushirikiano imara kati ya Menejimenti ya Halmashauri na wadau mbalimbali wa maendeleo.

Aidha amesisitiza kuwa mafanikio hayo yanaendelea kuimarisha uwajibikaji, uwazi na usimamizi bora wa rasilimali za umma kwa manufaa ya wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi.

Pia ameitaka Halmashauri kuendeleza juhudi hizo ili kudumisha viwango vya utendaji na utoaji bora wa huduma kwa wananchi.








Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali inaendelea kutekeleza miradi mikubwa ya maji ili kumaliza tatizo la upatikanaji wa maji safi na salama katika mikoa yote ya Zanzibar.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 15 Julai 2026, Ikulu Zanzibar, alipokutana na Waziri wa Maji, Nishati na Madini Zanzibar, Mhe. Nadir Abdullatif, pamoja na Waziri wa Maji wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jumaa Aweso.

Amesema miradi ya maji tayari imeanza kuleta matokeo katika mikoa ya Kaskazini Unguja, Kusini Unguja na Mjini Magharibi, huku akisisitiza matumizi ya teknolojia za kisasa na kuimarisha ushirikiano kati ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za maji.

Kwa upande wake, Waziri wa Maji wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jumaa Aweso, ameahidi kuendelea kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika utekelezaji wa miradi ya maji na kueleza kuwa wizara yake imeandaa mfumo wa kidijitali utakaowezesha wananchi kutoa taarifa za changamoto za huduma ya maji ili zipatiwe ufumbuzi kwa haraka.

Vilevile, amempongeza Rais Dkt. Mwinyi kwa utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo inayosimamiwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.










Na Oscar Assenga,MKINGA

JUMUIYA ya Afrika Mashariki (EAC) imeeleza itaendelea kuimarisha utekelezaji wa Mfumo Rahisi wa Biashara (Simplified Trade Regime-STR) ili kurahisisha biashara za mipakani, kuwawezesha wafanyabiashara wadogo kuongeza uzalishaji, kupanua masoko ya bidhaa zinazozalishwa ndani ya ukanda na kupunguza gharama za biashara.


Kauli hiyo ilitolewa na Naibu Katibu Mkuu wa EAC anayeshughulikia Forodha, Biashara na Fedha, Annette Semuwamba, wakati alipotembelea Kituo cha Huduma cha Pamoja Mpakani (One Stop Border Post-OSBP) cha Horohoro wilayani Mkinga, mkoani Tanga.


Ziara hiyo ni sehemu ya tathmini ya utekelezaji wa Mfumo Rahisi wa Biashara katika vituo saba vya Huduma vya Pamoja Mpakani vilivyopo ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Semuwamba alisema EAC itaendelea kushirikiana na nchi wanachama na wadau mbalimbali kuhakikisha wafanyabiashara wadogo wanaovuka mipaka wanapata mazingira rafiki kupitia taratibu rahisi za forodha.

“Tumefurahishwa kuona biashara kati ya nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki inaendelea kukua. Kinachotutia moyo zaidi ni kwamba bidhaa nyingi zinazovuka mipaka ni bidhaa zinazozalishwa ndani ya ukanda wetu,” alisema.

Alisema uwekezaji uliofanywa katika miundombinu ya vituo vya Huduma vya Pamoja Mipakani umechangia kupunguza muda wa kuhudumia mizigo na wasafiri, kupunguza gharama za biashara na kusaidia kushusha bei za bidhaa kwa walaji.

Aidha, aliipongeza Serikali ya Tanzania kwa kufunga mashine ya kisasa ya ukaguzi wa mizigo (scanner) katika mpaka wa Horohoro/Lunga Lunga, akisema hatua hiyo itaharakisha ukaguzi na uondoshaji wa mizigo.

Semuwamba alipendekeza pia kuanzishwa kwa mfumo wa kubadilishana picha za mizigo iliyokaguliwa kwa kutumia mashine hizo kati ya vituo vya Huduma vya Pamoja Mipakani ili kupunguza gharama za uwekezaji wa vifaa hivyo katika maeneo mengine ya mipakani.

Awali, Mkuu wa Kituo cha Huduma cha Pamoja Mpakani Horohoro, Shadrack Mbonea, alisema kituo hicho kimechangia kwa kiasi kikubwa kurahisisha biashara na usafirishaji wa mizigo kati ya Tanzania na Kenya.

Alisema Horohoro ni miongoni mwa vituo saba vya Huduma vya Pamoja Mipakani nchini vinavyowezesha wasafiri, magari na mizigo kupata huduma zote za mipakani katika eneo moja badala ya kuhudumiwa kila upande wa mpaka.

“Kituo hiki kilianza majaribio ya utoaji wa huduma kwa mfumo wa One Stop Border Post mwezi Septemba 2021 na tangu wakati huo kimeendelea kufanya kazi kwa mafanikio makubwa,” alisema.

Mbonea alisema kituo hicho kina taasisi 19 za Serikali zinazoongozwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), zikiwemo Idara ya Uhamiaji, Jeshi la Polisi, Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA), Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA), TASAC, Tume ya Madini, Idara ya Uvuvi, Idara ya Mifugo, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).

Alisema taasisi hizo zina jukumu la kukusanya mapato ya Serikali, kurahisisha biashara, kulinda jamii dhidi ya bidhaa hatarishi, kutekeleza sera za biashara, kukusanya takwimu za biashara za mipakani na kudhibiti magendo.

Kwa mujibu wa Mbonea, hapo awali mfumo wa OSBP ulikuwa ukifanya kazi kwa saa 12 kwa siku, hali iliyowalazimu wasafiri na wasafirishaji wa mizigo kukamilisha taratibu za forodha katika kila upande wa mpaka.

Alisema kupitia makubaliano kati ya Tanzania na Kenya, huduma sasa zinatolewa kwa saa 24, hatua iliyopunguza muda wa kusubiri na kuongeza ufanisi wa utoaji huduma.

Aidha, alisema kituo hicho kinatekeleza Mfumo Rahisi wa Biashara unaowawezesha wafanyabiashara wadogo wanaosafirisha bidhaa zenye thamani isiyozidi dola za Marekani 2,000 kutumia taratibu rahisi za forodha.

“Tumeanzisha dawati maalumu la kuwahudumia wafanyabiashara wadogo, tumerahisisha utaratibu wa ukadiriaji wa kodi kwa kutumia fomu ya F88 na tunatambua Vyeti Rahisi vya Asili ya Bidhaa vinavyotolewa na mamlaka za Kenya,” alisema.

Aliongeza kuwa kituo hicho pia kinatekeleza Mfumo wa Himaya Moja ya Forodha wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (Single Customs Territory-SCT), ambao umechangia kupunguza muda wa uondoshaji wa mizigo, kushusha gharama za biashara na kuondoa vikwazo vya biashara ndani ya ukanda.

Alisema ushirikiano kati ya Horohoro na Lunga Lunga umeimarisha mapambano dhidi ya magendo kupitia doria za pamoja, mikutano ya kila robo mwaka na utoaji wa elimu kwa wafanyabiashara kuhusu taratibu za biashara za mipakani.

Takwimu zinaonyesha kuwa thamani ya bidhaa zinazouzwa nje kupitia mpaka wa Horohoro/Lunga Lunga imeongezeka kutoka Sh milioni 306.4 mwaka wa fedha 2022/23 hadi Sh milioni 548 mwaka 2024/25. Aidha, thamani ya bidhaa zinazoingizwa nchini kupitia mpaka huo imeongezeka kutoka Sh milioni 134.7 hadi Sh milioni 175.9 katika kipindi hicho.

Ongezeko hilo linaakisi mafanikio ya juhudi za EAC na nchi wanachama katika kuimarisha biashara za mipakani, kuongeza ushindani wa bidhaa zinazozalishwa ndani ya ukanda na kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi kati ya Tanzania na Kenya.
Benki ya NMB imetwaa tuzo ya Best Bancassurance Innovation and Partner of the Year – Tanzania 2026 kutoka World Economic Magazine. Tuzo hiyo, iliyotangazwa na taasisi hiyo yenye makao Delaware, Marekani, imetambua matumizi ya teknolojia na ushirikiano wa NMB katika kupanua huduma za bima.

Kupitia chatbot ya JIRANI, wateja wanaweza kutumia WhatsApp kununua bima za magari na maisha ya vikundi, kuwasilisha nyaraka, kupata kumbukumbu za malipo na kuanzisha madai.

Aidha, UmeBima Mini App ndani ya NMB Mkononi Super App imeunganisha huduma za bima na shughuli nyingine za kila siku za kifedha.

Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB, Filbert Mponzi, alisema tuzo hiyo ni uthibitisho wa juhudi za benki na washirika wake katika kurahisisha upatikanaji wa bima na kuwafikia Watanzania wengi zaidi. Mkuu wa Idara ya Bima wa NMB, Martine Massawe, aliongeza kuwa huduma za JIRANI na UmeBima zimepunguza muda na hatua anazopitia mteja ili kupata huduma za bima.

Kwa zaidi ya wateja milioni 10, matawi 251 na vituo zaidi ya 75,000 vya NMB Wakala, benki hiyo ina mtandao mpana wa kufikisha bima kwa kaya, vikundi na biashara nchini. Hatua hiyo ni muhimu katika soko ambalo uwiano wa malipo ya bima kwa Pato la Taifa ulifikia asilimia 2.08 mwaka 2024.




Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe.Dkt. Mahmoud Thabit Kombo leo Julai 14, 2026 amekabidhiwa rasmi kombe kutoka kwa Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt  Ngwaru Maghembe linalotokana na ushindi wa timu ya Wanadiplomasia katika Bonanza Kuu la Bunge la Benki ya CRDB lililofanyika tarehe 20 Juni 2026 katika Uwanja wa Jamhuri, jijini Dodoma.

Timu ya Wanadiplomasia, iliyoshirikiana na wawakilishi kutoka Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, ilitwaa ubingwa baada ya kuishinda timu ya Wabunge kwa mikwaju ya penalti 5–4, kufuatia sare ya bao 1–1 katika muda wa kawaida wa mchezo.

Mechi hiyo ilikuwa kivutio kikuu cha bonanza hilo la michezo na afya, lililolenga kuimarisha afya, mshikamano na ushirikiano miongoni mwa viongozi na watumishi wa taasisi mbalimbali za umma. 

Aidha, ushindi wa timu hiyo ya Wanadiplomasia unaendelea kudhihirisha umuhimu wa michezo kama nyenzo ya kuimarisha mahusiano mema, urafiki na ushirikiano baina ya taasisi za Serikali na wadau wake.

Awali kombe hilo lilipokelewa na Mhe. Dkt. Ngwaru kwa niaba ya Mhe. Waziri Kombo kutoka kwa Mkuu wa Mabalozi ambaye ni Balozi wa Visiwa vya Comoro nchini, Mhe. Dkt. Ahamada El Badaoui Mohamed Fakih.









ZAIDI ya wananchi 8,000 kutoka Mkoa wa Arusha na maeneo mengine nchini wamepata huduma za uchunguzi na matibabu bila malipo katika siku mbili za kwanza za kambi maalumu ya afya inayofanyika jijini Arusha. Kambi hiyo ya siku saba ilianza Julai 13, 2026 na itahitimishwa Julai 19, ambapo wananchi wanapatiwa vipimo, ushauri wa madaktari bingwa, matibabu, dawa na rufaa bila malipo.

Kambi hiyo imeandaliwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha kwa kushirikiana na Ofisi ya Mbunge wa Arusha Mjini, Paul  Makonda, pamoja na Wizara ya Afya, hospitali za rufaa za kitaifa, taasisi maalumu za afya na hospitali binafsi. Katika siku ya kwanza wananchi 3,500 walihudumiwa, huku zaidi ya 4,500 wakipata huduma siku ya pili na kufanya jumla ya walionufaika kufikia zaidi ya 8,000.

Huduma zinazotolewa ni pamoja na vipimo mbalimbali vya afya, ushauri wa kitaalamu, matibabu, dawa na rufaa. Aidha, zaidi ya watu 50 walijitokeza kuchangia damu katika banda la Mpango wa Taifa wa Damu Salama, huku wagonjwa waliobainika kuhitaji matibabu ya kina wakipelekwa hospitalini kwa magari ya wagonjwa.

Akizungumza katika kambi hiyo, Makonda alimshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Wizara ya Afya, madaktari, taasisi za afya na sekta binafsi kwa kuwezesha huduma za kibingwa kuwafikia wananchi wa Arusha na maeneo ya jirani. Alisema mafanikio hayo yametokana na ushirikiano mzuri kati ya Serikali, viongozi wa wananchi, hospitali za rufaa na wadau wa sekta ya afya.

Makonda alisema wananchi wengi wanaofika kambini hawana uwezo wa kumudu gharama za vipimo na matibabu katika mazingira ya kawaida, huku baadhi wakishindwa kuendelea na matibabu baada ya fedha zao kuishia kwenye vipimo vya awali.

Alieleza kuwa ingawa wananchi wanapata huduma hizo bila malipo, taasisi, hospitali, madaktari na wadau wameingia gharama kubwa za usafiri, vifaa vya uchunguzi, dawa, miwani, malazi, chakula na mahitaji mengine muhimu ili kuhakikisha huduma zinawafikia wananchi.

Aliwasihi wananchi wanaopewa dawa, miwani na maelekezo ya matibabu kuyafuata kikamilifu, akisisitiza kuwa dawa na huduma zote zilizotolewa zimegharimiwa na hivyo ni muhimu zitumike ipasavyo ili kuleta matokeo yaliyokusudiwa.

Pia aliwahimiza wafanyabiashara, wamachinga, waendesha bodaboda na bajaji pamoja na wananchi wengine kutenga muda wa kupima afya, akisisitiza kuwa huduma hizo zinapatikana kwa watu wote bila kujali wanakotoka, dini, kabila, chama cha siasa au hali yao ya kiuchumi.





Na Peter Haule na Joseph Mahumi, WF, Tanga

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amesema Serikali itafuatilia kwa karibu changamoto zinazokwamisha utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa barabara ya Pangani-Tanga  ili kuhakikisha unakamilika kwa wakati na kuanza kutoa huduma kwa wananchi pamoja na kuchochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi.

Mhe. Balozi Omar alitoa kauli hiyo alipotembelea mradi wa ujenzi wa sehemu ya barabara ya Pangani mkoani Tanga yenye urefu wa kilometa 50 kwa kiwango cha lami, ambayo ni sehemu ya mradi mkubwa wa barabara ya Bagamoyo (Makurunge)–Saadani–Pangani yenye urefu wa kilometa 256.

Ziara hiyo inafuatia kilio cha uongozi wa mkoa na  Wilaya ya Tanga pamoja na wakazi wa Wilaya ya Tanga wanaoathirika na ubovu wa barabara hiyo unaokwamisha shughuli zao za kiuchumi hususan wakati wa mvua na masika.

Alisema mradi huo umechelewa kukamilika kwa muda mrefu, hali inayolazimu Serikali kuangalia kwa kina changamoto zinazouchelewesha ili kuhakikisha unakamilika na wananchi wanaanza kunufaika na huduma za usafiri na usafirishaji.

"Mradi huu ni muhimu kwa maendeleo ya wananchi na uchumi wa nchi. Tutafuatilia changamoto zinazoukabili ili utekelezaji wake ukamilike kwa wakati na uweze kutoa huduma iliyokusudiwa," alisema Mhe. Balozi Omar.

Kwa upande wake, Kaimu Meneja wa Wakala wa Barabara nchini-TANROADS Mkoa wa Tanga, Bw. Jotrevas August, alisema kuwa Mkandarasi anasuasua kukamilisha mradi licha ya juhudi za Serikali kuwataka watekeleze ujenzi wa mradi huo kwa wakati. 

Alisema kuwa mazungumzo yanaendelea kati ya Serikali na Mkandarasi huyo, ambaye ni Kampuni ya ujenzi ya CHICO kutoka China ili atafute rasilimali fedha kwa ajili ya kukamilisha mradi huo.

Alisema hadi sasa kazi mbalimbali zimeendelea vizuri, ikiwemo kusafisha eneo la barabara kwa urefu wa kilometa 44.45, sawa na asilimia 88.9 ya kazi hiyo. 

Aidha, ujenzi wa madaraja pamoja na matengenezo ya barabara ya awali na ya mchepuko kwa kiwango cha changarawe unaendelea sambamba na hatua nyingine za utekelezaji wa mradi.

Bw. August alisema kuwa mradi huo utakuwa kiungo muhimu kinachounganisha Bandari za Dar es Salaam, Tanga na Mombasa, hatua itakayoongeza ufanisi wa biashara na usafirishaji katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Mradi wa barabara ya Bagamoyo (Makurunge)-Saadani-Pangani unatarajiwa kuwa moja ya miundombinu muhimu ya kimkakati itakayorahisisha usafiri, kuimarisha biashara na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika ukanda wa pwani na nchi jirani za Afrika Mashariki.












Na Mwandishi wetu, Mirerani

KAMPUNI ya Franone Mining & Gem LTD imenufaisha jamii mbalimbali Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, kupitia miradi tofauti ya maendeleo ikiwemo ya sekta ya elimu, afya na miundombinu, kupitia uwajibikaji kwa jamii (CSR).

Meneja wa kampuni ya Franone Mining & Gem LTD, Sweetbert Arbogast ameeleza hayo kwenye ziara ya ujumbe wa shirika la Miss World ulipotembelea eneo la madini ya Tanzanite kitalu C mji mdogo wa Mirerani.

Ujumbe huo uliongozwa na Mwenyekiti na Mkurugenzi mtendaji wa shirika la Miss World, Julia Morley lenye makao makuu yake jijini London, Uingereza na mnyange Miss World Africa 2025 Hasset Dereje wa Ethiopia.

Arbogast ameeleza kuwa miradi hiyo iliyotekelezwa na Franone Mining kwa ajili ya kusaidia jamii imefanyika katika maeneo mbalimbali ya wilaya ya Simanjiro.

Ametaja baadhi ya mradi hiyo ni ujenzi wa zahanati kwenye migodi ya madini ya Tanzanite na ukarabati wa barabara ya kilomita nane inayopanda kwenye machimbo hayo.

"Pia Franone imetoa madawati 100 kwa shule ya sekondari Mirerani B.W.Mkapa, ujenzi wa miundombinu ya madarasa shule ya sekondari Naisinyai na ujenzi wa miundombinu ya kituo cha afya Mirerani," amesema Arbogast.

Ameeleza kuwa kwenye kipindi cha mafuriko yaliyotokea mwaka 2024 walitoa msaada wa chakula kwenye Tarafa ya Moipo na Kata ya Msitu wa Tembo na wanafunzi wa shule ya msingi Oloshonyokie.

Ofisa madini mkazi Mirerani (RMO) George Kaseza amesema eneo tengefu la Mirerani kuna vitalu mbalimbali vinavyochimbwa madini ya vito ya Tanzanite.

Kaseza ameeleza kwamba sehemu hiyo ina maeneo tofauti ambapo kuna kitalu A, B, C na D ambapo wachimbaji wenye migodi wamepewa leseni za kuchimba madini ya Tanzanite.

Katibu wa chama cha wachimbaji madini mkoa wa Manyara (MAREMA) Tawi la Mirerani Rachel Njau amesema ugeni huo ni mzuri kwao kwani utatumika kutangazwa zaidi kwa madini hayo ya vito ya Tanzanite kimataifa.

Mwenyekiti wa wanawake wafanyabiashara wa magonga, Magreth Sogweda, amesema wamepata faraja kutembelewa na ugeni huo kwani wameongezewa nguvu na moyo zaidi wa kazi wanazozifanya zinazidi kuthaminiwa.

Mwenyekiti wa chama cha wafanyabiashara wa madini mkoa wa Manyara, (Magebomita) Mokia Ole Mrefu amesema ugeni huo ni wakimataifa hivyo ni fursa nzuri kwa madini ya Tanzanite kuzidi kutangazwa na kufahamika zaidi.



Top News