Na. Edmund Salaho - Dodoma

Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) limeendelea kuimarisha safu yake ya Uongozi ili kuboresha utendaji kazi wa Shirika hilo kwa kuwaapisha na kuwavisha vyeo Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi (1) Makamishna Wasaidizi wa Uhifadhi (3) pamoja na Afisa Uhifadhi Mkuu (1) zoezi ambalo limefanyika leo Aprili 25, 2026 katika Ofisi Kiunganishi za TANAPA jijini, Dodoma.

Akizungumza katika hafla hiyo ya kuwavisha vyeo Makamishna hao Kamishna wa Uhifadhi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) Musa Nassoro Kuji,alitoa msisitizo kwa Makamishna hao kufanya Kazi kwa bidii, weledi na kusikiliza watu wanaowaongoza ili kuleta tija zaidi pamoja na kufikia malengo ya Shirika na Taifa kwa ujumla.

"Nendeni mkachape kazi kwa bidii na weledi huku mkiishi viapo vyenu mlivyoapa leo. Kiongozi mzuri ni yule anaesikiliza mawazo ya watu wake anaowaongoza hivyo, mkasikilize watu mnaowaongoza" alisisitiza Kamishna Kuji.

Akitoa shukurani kwa niaba ya Makamishna wapya, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi, Abdallah Omary Kiwango alishukuru Bodi ya Wadhamini TANAPA pamoja na Uongozi wa Shirika kwa imani kubwa walionayo juu yao.

"Napenda kuchukua nafasi hii kwa niaba ya Makamishna wenzangu  kuishukuru Bodi ya Wadhamini na Uongozi wa Shirika kwa kutuamini na kutukabidhi majukumu haya kama tulivyotoka kuapa, tunaahidi kufanya kazi kwa bidii na weledi wa hali ya juu ili kufanikisha malengo ya Taasisi ya kuendeleza Uhifadhi endelevu na kukuza Utalii katika Hifadhi za Taifa"

"Leo sio mwisho wa safari bali ni mwanzo wa dhamira mpya. Tunachukua majukumu haya tukiwa na nia thabiti ya kufanya kazi kwa weledi, nidhamu na uadilifu wa hali ya juu. Tuko tayari kujitoa kwa nguvu zote kuhakikisha tunalinda rasilimali za Taifa letu kwa faida ya kizazi cha sasa na kijacho" alisema Kamishna Kiwango

Makamishna wa Uhifadhi walioapishwa leo ni Abdallah Omary Kiwango ambaye ameapishwa kuwa Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi, Makamishna Wasaidizi wa Uhifadhi, Philbert  Michael Ngoti, Joachim Shaaban Tesha, Michael Joseph Tarimo pamoja na Afisa Uhifadhi Mkuu, Manendo Peter Maziku.







Na Janeth Raphael MichuziTv 


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amesema uzinduzi wa meli ya kwanza ya uvuvi wa bahari kuu ya Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO) ni hatua muhimu inayoweka msingi imara wa utekelezaji wa sera na mikakati ya nchi katika kuendeleza sekta ya uvuvi na kukuza uchumi wa buluu.

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya uzinduzi wa meli hiyo, Rais Samia alisema hatua hiyo ni sehemu ya mabadiliko ya kimkakati katika usimamizi na udhibiti wa rasilimali za bahari kuu, huku ikilenga kuongeza mchango wa sekta ya uvuvi katika uchumi wa taifa.

Rais Samia amesema Serikali imejidhatiti kulifufua na kuliimarisha Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO) ili liweze kushiriki kikamilifu katika kusimamia na kunufaika na rasilimali zilizopo katika bahari kuu kwa manufaa ya Watanzania wote.

Ameongeza kuwa uzinduzi wa meli hiyo unaakisi maono mapya ya Serikali katika kuhakikisha rasilimali za bahari zinasimamiwa kwa tija, uwazi na ufanisi zaidi, ili kuongeza mapato ya taifa na ajira kwa wananchi.

Katika hotuba yake, Rais Samia pia amesisitiza dhamira ya Serikali ya kuendelea kuimarisha taasisi nyingine za udhibiti na usimamizi wa rasilimali za uvuvi ili kukabiliana na changamoto ya uvuvi haramu unaoharibu mazingira na kuhatarisha uhai wa viumbe vya majini.

Amesema Serikali itaendelea kuchukua hatua madhubuti za kukomesha uvuvi usiozingatia sheria na taratibu, ili kuhakikisha uendelevu wa rasilimali za bahari kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

Aidha, Rais Samia amesema Serikali imefanya jitihada kubwa kuboresha mazingira ya shughuli za uvuvi katika maziwa na bahari kwa kuwezesha upatikanaji wa mitaji, utaalamu na vifaa, ikiwemo boti za kisasa za uvuvi pamoja na kuendeleza teknolojia za ufugaji samaki kwa njia ya vizimba.

Uzinduzi wa meli hiyo ya kwanza ya uvuvi wa bahari kuu kwa TAFICO unatajwa kuwa hatua muhimu katika kuimarisha sekta ya uvuvi nchini na kuongeza uwezo wa Tanzania kunufaika na uchumi wa buluu kupitia rasilimali zake za baharini.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akibonyeza Kitufe kuashiria Uzinduzi wa Meli ya Kwanza ya Uvuvi wa Bahari Kuu kwenye hafla fupi iliyofanyika katika Makao Makuu ya Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO) Kigamboni Jijini Dar es Salaam tarehe 25 Aprili, 2026.





 

-Pia mapato yaongezeka yafikia bilioni 640.5 katika kipindi cha miaka minne

Na Said Mwishehe,Michuzi TV-Dodoma

BOHARI ya Dawa(MSD) ambayo ni taasisi iliyoundwa kisheria mwaka 1993 ikifuatiwa na maboresho mbalimbali ya sheria ili kuiwezesha kutekeleza majukumu yake ya msingi imeendelea kujivunia mafanikio yaliyopatikana katika utoaji huduma za afya nchini.

Akizungumza leo Aprili 24,2026 wakati wa kikao kazi kilichoandaliwa na MSD na kuhusisha Wahariri na waandishi wa habari Mfamasia kutoka kitlendi cha Mipango,Ufuatiliaji na Tathimini Lilian Magesa kutoka MSD ametumia nafasi hiyo kuelezea kuwa kumekuwepo na mafanikio katika kipindi cha miaka minne 2021/22 hadi mwaka 2024/25.

Amefafanua katika kipindi cha miaka minne mapato ya MSD yameongezeka kwa asilimia 103 kutoka Sh.Bilioni 315.12 hadi kufikia kiasi cha Sh.Bilioni 640,5 mwaka 2024/25.

Pia mafanikio mengine ni kuongezeka kwa upatikanaji wa bidhaa za afya ashiri kutoka asilimia 42 mwaka 2021/22
hadi kufika asilimia 73 Machi, 2026.


“Hali ya utimizaji wa mahitaji wa vituo vya kutolea huduma za afya umeendelea kuongezeka kutoka asilimia 4l hadi kufikia asilimia 77 katika kipindi cha miaka minne.”

Pia amesema mafanikio mengine ni kuongezeka kwa mizunguko ya usambazaji wa bidhaa za afya kwenda vituo vya kutolea
huduma za afya kutoka mizunguko minne kwenda mizunguko sita kwa mwaka huku ununuzi wa bidhaa za kuwezesha uzazi pingamizi ( CEmONO) umefikia asilimia 100 ya
MS.

Ameongeza kuwa mafanikio mengine mashine 162 za kusafisha damu(dialysis) zimesambazwa kutoka mashine 60 mwaka 2021/2022 zilizogharimu Sh.bilioni 10.14

Pia kukamilisha ujenzi wa maghala ya kisasa yanayokidhi viwango vya uhifadhi na kuanza kutumika katika Kanda ya Dodoma na Mtwara -mita za mraba 12,000.Aidha kuanza kwa ujenzi wa ghala la Chato mkoani Geita lilifikia asilimia 42 ya utekelezaji.

Mafanikio mengine ni uanzishwaji wa kampuni tanzu ijulikanayo kama MSD Medipharm Manufacturing Company yenye jukumu la kusimamia uzalishaji unaotekelezwa kibiqshara na kwa ufanisi mkubwa .

“Pia kiwanda cha mipira ya mikono -Idofi kukamilika na kuanza kazi rasmi ya uzalishaji Februari 2024 pamoja na ongezeko la thamani ya bidhaa zinazonunuliwa kutoka kwa wazalishaji wa ndani kutoka Sh.bilioni 15.90 zilizonunuliwa mwaka 2021/22 hadi Sh.bilioni 98.72 mwaka 20/2024/25, ”amesema. 

Kuhusu changamoto amesema mojawapo ni uhaba wa mtaji wa kuwezesha;Ununuzi wa bidhaa za Afya toshelevu kwa kiwango cha miezi 5, Ujenzi wa miundombinu toshelezi na inayokidhi viwango vya uhifadhi pamoja na ushiriki na uanzishai wa viwanda vya bidhaa za afya.

Pia uwepo wa madeni, Washitiri kuchelewa kuleta bidhaa za afya kulingana na mikataba,ufinyu wa maeneo ya kuhifadhia bidhaa za Afya licha ya kuongezeka kwa idadi ya watu na mahitail na utegemezi wa uagizaji kutoka nje ya nchi kutokana na uwezo hafifu wa viwanda vya ndani.








Serikali kupitia Tume ya Madini imesema itaendelea kutoa bei elekezi za madini ya dhahabu, shaba na fedha kila siku itakayotumika kwenye masoko na vituo vya ununuzi wa madini hatua inayolenga kuongeza uwazi katika biashara ya madini na kuwawezesha wachimbaji kuuza madini yao kwa bei halisi ya soko la dunia.

Akifunga mafunzo kwa Mameneja na Wakaguzi Wakuu wa Migodi ya uchimbaji mdogo kutoka mikoa ya kimadini ya Kahama, Mbogwe na Shinyanga mapema jana, Mkurugenzi wa Ukaguzi na Biashara ya Madini, CPA Venance Kasiki alisema taarifa hizo za bei zitawasaidia wachimbaji kufanya maamuzi sahihi ya biashara na kuepuka hasara zitokanazo na madalali maarufu kama vishoka.

Alisema hapo awali baadhi ya wachimbaji walikuwa wakiuza madini bila kufahamu bei halisi ya soko la dunia, hali iliyosababisha kupoteza mapato na kuingia katika mikataba isiyo na manufaa.

Alifafanua kuwa kwa sasa bei za madini hutolewa kila siku, hivyo mchimbaji ana uwezo wa kufanya uamuzi sahihi kabla ya kuuza madini yake.

Aidha, alisema Serikali inaendelea kuimarisha mifumo ya uwazi katika biashara ya madini pamoja na kuwahamasisha wananchi kutoa taarifa za vitendo vya utoroshaji wa madini, ambapo watoa taarifa watapatiwa zawadi maalum.

CPA Kasiki alionya kuwa watakaobainika kujihusisha na utoroshaji wa madini watakabiliwa na hatua kali za kisheria ikiwemo kufunguliwa mashitaka, kutaifishwa madini, kulipa faini pamoja na kifungo kwa mujibu wa sheria.

Katika hatua nyingine, alisisitiza umuhimu wa kuzingatia usalama migodini, akibainisha kuwa uchimbaji usiofuata taratibu hauwezi kuwa endelevu, huku akisisitiza kuwa uhai wa binadamu una thamani kubwa kuliko madini.

Aliwahimiza wachimbaji kutumia maabara ya Tume ya Madini katika kupima sampuli ili kufanya maamuzi sahihi badala ya kutumia maabara zisizotambulika.

Aidha, aliwakumbusha wamiliki wa leseni kufanya miradi endelevu kwa jamii zinazozunguka migodi ikiwa ni utekelezaji wa takwa la Kisheria la wajibu wa mwenye leseni kwa jamii (CSR).

Awali, Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Migodi na Mazingira, Mhandisi Hamisi Kamando alisema mwitikio wa washiriki ulikuwa mkubwa ambapo kati ya washiriki 400 waliotarajiwa, washiriki 370 walijitokeza, jambo linaloonesha hamasa kubwa ya wachimbaji kujifunza masuala ya usalama, afya na utunzaji wa mazingira.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa SHIREMA, Hamza Tandiko alisema mafunzo hayo yameongeza uelewa wa wachimbaji katika biashara ya madini, matumizi salama ya kemikali na baruti, uhifadhi wa mazingira pamoja na uchunguzi wa ajali migodini, akisisitiza umuhimu wa kuachana na uchimbaji wa kubahatisha na kuingia katika uchimbaji wa kisasa na wenye tija.




 

Na Augusta Njoji

Timu ya wataalamu wa afya kutoka Hospitali ya Halmashauri ya Mji Handeni imeanza rasmi mpango wa utoaji elimu kwa jamii ili kuimarisha kinga dhidi ya magonjwa na kuboresha ustawi wa wananchi.

Utoaji wa elimu hiyo imejikita katika afua za kuzuia malaria, lishe bora, bima ya afya kwa wote pamoja na huduma za mama na mtoto, ikiwa ni sehemu ya jitihada za serikali kuhakikisha jamii inakuwa na afya bora.

Akizungumza kuhusu zoezi hilo, Ofisa Afya wa Halmashauri na Mratibu wa Elimu ya Afya kwa Umma, Jonas Mkondya, amesema wamejipanga kutembelea kila mtaa katika kata zote 12 za Halmashauri ya Mji Handeni ili kuwafikia wananchi wengi zaidi na kuwapatia elimu sahihi ya afya.

Ameeleza kuwa elimu hiyo itasaidia kuongeza uelewa kwa wananchi juu ya namna ya kujikinga na magonjwa, kuboresha lishe pamoja na umuhimu wa kujiunga na bima ya afya kwa wote ili kupata huduma kwa urahisi.

Kata zitakazofikiwa katika ziara hiyo ya wataalamu wa afya ni Konje, Mabanda, Kwenjugo, Malezi, Chanika, Mlimani, Mdoe, Vibaoni, Kwediyamba, Kideleko, Msasa na Kwamagome.

Na Mwandishi Wetu 

IMEELEZWA kuwa Maji ya kimataifa ni moja ya rasilimali inayoleta amani katika nchi mbalimbali zinazonufaika na wananchi wake.

Waziri wa Maji Jumaa Aweso akifungua kikao cha 13 cha  Baraza la Mawaziri la Kamisheni ya Bonde la Mto Zambezi (ZAMCOM) jijini Dar es salaam amesema maji hayana mpaka na yanakusanya watu kwa maendeleo yao.

Aweso ambaye katika mkutano huo ni Mwenyekiti ameainisha kuwa umoja wa wananchi na nchi walizopo umeletwa na maji ya kimataifa, maji yanayovuka mipaka ya nchi zao.

Amesema ni muhimu kuwa na rasilimali za kutosha ili kuleta maendeleo na wananchi wanashirikishwa kutunza rasilimali za maji ili kuleta maendeleo katika sekta nyingine za uchumi.

Waziri Aweso amesisitiza kwa wajumbe wa mkutano huo kuwa maji ni muhimu na yanahitajika kuleta maendeleo kwa wananchi.

ZAMCOM inagusa maisha ya kila wananchi zaidi ya milioni 51 na imekusanya nchi za Tanzania, Angola, Zambia, Malawi, Namibia, Botswana, Zimbabwe, na Msumbiji.







Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ametoa wito kwa Wakazi wa Dunga mkoa wa Kusini Unguja kuendelea kushirikiana na Idara ya Uhamiaji pamoja na Vyombo vingine vya Ulinzi na Usalama, katika kuhakikisha amani inaendelea kushamiri nchini.

Makamu wa Rais ametoa wito huo wakati wa hafla ya uzinduzi wa Afisi ya Uhamiaji Wilaya ya Kati mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar katika hafla iliyofanyika katika eneo Dunga. 

Amewasihi kushirikiana na Serikali kwa njia ya kutoa taarifa mbalimbali kuhusu wahamiaji haramu, watu wanaoishi nchini kinyume cha sheria, au wanaojihusisha na shughuli haramu zilizo kinyume na malengo ya ukaazi wao. Makamu wa Rais amesema amani na umoja ni Tunu za Taifa, ambayo kila mtanzania anapaswa kuilinda.  

 Makamu wa Rais amewasihi wananchi wote kuendelea kuunga mkono juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mheshimiwa Dkt. Hussein Ali Mwinyi, kwa jitihada kubwa wanazozifanya katika kuiletea nchi maendeleo ili kwa pamoja kuweza kufikia malengo ya kuboresha maisha ya kila Mtanzania na kuiletea maendeleo nchi.

 Halikadhalika, Makamu wa Rais ametoa rai kwa Taasisi za Serikali kuendelea kuwaamini na kuwapa watanzania wazawa kazi za ujenzi ili waendelee kupata uwezo wa kiteknolojia na kifedha. 

Makamu wa Rais ameipongeza Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kupitia Idara ya uhamiaji kwa kutoa kandarasi kwa mtanzania mzawa katika ujenzi wa jengo la Afisi ya Uhamiaji Wilaya ya Kati, Unguja.

 Aidha, Makamu wa Rais amesema Serikali imejikita katika kuimarisha huduma za uhamiaji kwa kuboresha vitendea kazi na miundombinu kwa ujumla. Ameongeza kwamba Ujenzi wa Afisi za Uhamiaji za Wilaya ni njia mojawapo ya jitihada za kufikia azma hiyo. 

Sambamba na uboreshwaji wa Miundombinu ya Majengo, Serikali imeweka mkazo katika utoaji wa Mafunzo kwa watumishi, kusimamia stahiki za Watumishi, na kufanya maboresho ya mara kwa mara ya Sheria na Kanuni za Uhamiaji nchini. 

Vilevile, Makamu wa Rais amesema huduma za Kiuhamiaji Zanzibar ni muhimu na ni chachu katika kukuza sekta ya biashara, uwekezaji na utalii, kwa kuzingatia ongezeko kubwa la Wageni wanaotembelea Zanzibar, hususan katika kipindi ambacho Serikali zote mbili zimejikita kukuza Sekta ya Utalii kufuatia uzinduzi wa Filamu maarufu ya Royal Tour.

Makamu wa Rais amesema Mapinduzi ya mwaka 1964 yaliyoongozwa na Rais wa kwanza wa Zanzibar, Hayati Mzee Abeid Amani Karume yana historia kubwa kwa Zanzibar na watu wake. 

Tangu wakati huo, Mapinduzi hayo yameijengea heshima kubwa Zanzibar na kuwapa Wazanzibari wigo mpana wa kufanya maamuzi kuhusu maisha yao wenyewe na kujiletea maendeleo.

 Amesema pia Muungano umeimarisha zaidi umoja, mshikamano na kudumisha amani na utulivu, na kuchochea maendeleo kwa wananchi wote. Amesema Baada ya Mapinduzi na Muungano, huduma mbalimbali za jamii kama vile afya na elimu zilifunguka kwa wananchi wote. 

Jengo hilo la Afisi ya Uhamiaji Wilaya ya Kati limegharimu shilingi bilioni 2.1.










Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Mpango wa Maendeleo ya Jamii kupitia Mfuko wa TASAF umeendelea kuonesha mchango mkubwa katika kuboresha huduma za afya nchini, ambapo katika Kijiji cha Mgunga, Kata ya Msamalo wilayani Chamwino mkoani Dodoma, wananchi wameeleza kufurahishwa na hatua ya ujenzi wa Kituo cha Afya Msamalo huku wakitoa ombi la kukamilishwa kwa majengo muhimu ya huduma za upasuaji na mama na mtoto ili kuongeza ufanisi wa huduma.

Hali hiyo imebainishwa wakati wa ziara ya wataalamu na wawakilishi kutoka Ubalozi wa Uswisi nchini Tanzania waliotembelea eneo hilo kwa lengo la kukagua maendeleo ya utekelezaji wa awamu ya pili ya mpango wa TASAF pamoja na kujionea namna mradi wa kituo hicho cha afya unavyoendelea kunufaisha jamii ya maeneo ya jirani.

Katika maelezo yao, wananchi wamesema uwepo wa kituo hicho umekuwa mkombozi mkubwa, lakini bado changamoto ya kukosekana kwa huduma za upasuaji na wodi ya mama na mtoto imeendelea kuwalazimu kusafiri umbali mrefu kufuata huduma katika hospitali za wilaya na rufaa, jambo linaloongeza gharama na wakati wa kupata matibabu.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Mgunga, Simon Masagasi, amesema ujenzi wa kituo hicho umekuwa hatua muhimu kwa maendeleo ya afya ya jamii, lakini bado kuna hitaji kubwa la kukamilisha miundombinu iliyobaki ili kituo kiweze kutoa huduma zote muhimu kwa wakazi wa eneo hilo na vijiji jirani.

Alieleza kuwa kabla ya uwepo wa kituo hicho, wananchi, hususan wajawazito, walilazimika kutumia usafiri wa mbali na wakati mwingine usio salama kufuata huduma, hali iliyokuwa ikiweka maisha yao hatarini.

Mkazi wa eneo hilo, Mary Sabugo, amesema awali changamoto ya huduma za afya ilikuwa kubwa zaidi, kwani walilazimika kusafiri kwenda maeneo ya mbali hata kwa matatizo madogo ya kiafya, jambo lililokuwa likichelewesha matibabu na kuongeza hatari kwa wagonjwa.

Kwa upande wake, Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Msamalo, Rebecca Kitundu, amesema kituo hicho kinahudumia zaidi ya wakazi 16,000 kutoka kata za Msamalo, Ikoa na Igandu, hivyo ongezeko la huduma linahitaji miundombinu imara zaidi ili kukidhi mahitaji ya wananchi.

Amefafanua kuwa kukamilika kwa majengo ya upasuaji na huduma za mama na mtoto kutasaidia kupunguza msongamano wa wagonjwa pamoja na kupunguza rufaa zisizo za lazima kwenda hospitali za mbali.

“Tunashukuru kwa hatua iliyofikiwa kupitia TASAF, lakini bado tunaiomba Serikali na wadau wa maendeleo kuhakikisha miundombinu iliyobaki inakamilishwa ili huduma ziwe bora zaidi,” alisema Kitundu.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ukaguzi wa Ndani, Uswege Edward, aliipongeza Serikali kwa ushirikiano wake katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo kupitia TASAF, akisema umeleta mabadiliko chanya katika sekta mbalimbali ikiwemo afya.

Alibainisha kuwa awamu ya pili ya mpango huo imewezesha uboreshaji wa huduma za jamii katika maeneo mengi nchini, huku akishukuru pia wadau wa maendeleo wakiwemo Ubalozi wa Uswisi kwa kuendelea kufuatilia na kushirikiana katika miradi hiyo.

Aidha, aliwahimiza wananchi waliopitia katika mpango huo na kufikia hatua ya kujikwamua kiuchumi kuendelea kushiriki shughuli za uzalishaji mali ili kudumisha mafanikio yaliyopatikana kupitia programu hiyo ya kijamii.

Serikali imetangaza kuwa awamu ya tatu ya Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini kupitia TASAF inatarajiwa kuanza kutekelezwa hivi karibuni katika maeneo mbalimbali nchini, hatua inayotarajiwa kuongeza wigo wa miradi ya maendeleo na kuimarisha zaidi huduma za msingi kwa wananchi, hususan katika sekta za afya, elimu na miundombinu ya kijamii.










Top News