Na Mwandishi Wetu.
Wabunge
wameipongeza Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) kwa kuendelea
kupanua wigo wa huduma za hifadhi ya jamii kupitia Skimu ya Hifadhi kwa
Wananchi Waliojiajiri, wakisema mpango huo unatoa fursa kwa mamilioni ya
Watanzania kunufaika na huduma za hifadhi ya jamii.
Aidha,
wamepongeza uwekezaji uliofanywa na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa
Watumishi wa Umma (PSSSF) katika Kiwanda cha Kimataifa cha Bidhaa za
Ngozi cha Kilimanjaro (KLICL), wakisema mradi huo una mchango mkubwa
katika kukuza viwanda, kuongeza thamani ya mazao ya mifugo na
kutengeneza ajira.
Pongezi hizo
zilitolewa jijini Dodoma wakati wa semina ya wabunge kuhusu Skimu ya
Hifadhi kwa Wananchi Waliojiajiri na Mradi wa Kiwanda cha Kimataifa cha
Bidhaa za Ngozi cha Kilimanjaro.
Akizungumza
kwa niaba ya Spika wa Bunge, Mhe. Mussa Azzan Zungu, Naibu Spika wa
Bunge, Mhe. Daniel Sillo, aliipongeza NSSF pamoja na PSSSF kwa kuendelea
kutoa elimu kwa wabunge kuhusu masuala ya hifadhi ya jamii na miradi
mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa na mifuko hiyo.
Mhe.
Sillo alisema elimu hiyo ni muhimu kwa wabunge kwani itawawezesha kuwa
mabalozi wa kuhamasisha wananchi katika majimbo yao kujiunga na mifumo
ya hifadhi ya jamii na kufahamu uwekezaji unaofanywa na mifuko hiyo.
Baadhi
ya wabunge walioshiriki semina hiyo, akiwemo Mhe. Said Salimu na Mhe.
Rashid Shangazi, waliipongeza NSSF kwa juhudi zake za kuwafikia wananchi
waliojiajiri na kuimarisha huduma za hifadhi ya jamii nchini.
Walisema
skimu hiyo itasaidia kujenga utamaduni wa kuweka akiba, kuongeza
usalama wa kipato na kuwapa wananchi waliojiajiri fursa ya kunufaika na
huduma za hifadhi ya jamii.
Kwa upande
wa uwekezaji wa PSSSF, wabunge Jackson Kiswaga na Rashid Shangazi
waliipongeza PSSSF kwa uwekezaji kwenye kiwanda hicho, huku wakiishauri
sekta binafsi ikaribushwe katika uendeshaji wa kiwanda ili kuongeza
nguvu katika masoko na uzalishaji.
Kwa
upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na
Mahusiano, Mhe. Deus Sangu, alisema Serikali inaendelea kuimarisha
huduma za hifadhi ya jamii kwa kuwajumuisha wananchi waliojiajiri, ambao
kwa muda mrefu walikuwa nje ya mifumo rasmi ya hifadhi ya jamii licha
ya mchango wao mkubwa katika uchumi wa taifa.
Kuhusu
PSSSF, Mhe. Sangu alisema mradi wa kiwanda hicho unamilikiwa kwa ubia
kati ya Mfuko huo na Jeshi la Magereza kupitia kampuni yake ya Prisons
Corporation Sole (PCS) na kuwa umekuwa na manufaa makubwa kwa jamii na
taifa kwa ujumla.
Awali, Mkurugenzi
Mkuu wa NSSF, Bw. Masha Mshomba, alisema mfuko huo unalenga kuandikisha
wananchi waliojiajiri milioni 3.7 ifikapo Juni 2031 kupitia Skimu ya
Hifadhi ya Jamii. Alisema takribani asilimia 85 ya nguvu kazi nchini,
sawa na wananchi milioni 20.98 wenye uwezo wa kufanya kazi, wamejiajiri,
jambo linaloifanya skimu hiyo kuwa nyenzo muhimu ya kuwafikia makundi
mbalimbali ya wananchi.
Bw. Mshomba
alisema wanachama wa skimu hiyo watanufaika na mafao mbalimbali yakiwemo
pensheni ya uzee, mafao ya urithi, ulemavu, uzazi na matibabu. Alisema
wananchi sasa wanaweza kujiunga, kuchangia na kufuatilia taarifa zao kwa
njia za kidijitali kupitia simu za mkononi, huku kiwango cha chini cha
mchango kikiwa shilingi 30,000 kwa mwezi.
Naye,
Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF, Bw. Fortunatus Magambo, amesema kiwanda hicho
kinazalisha bidhaa zenye ubora wa hali ya juu na kimekuwa na mchango
mkubwa kwa jamii na taifa kwa ujumla.
Alisema
kiwanda hicho kimeongeza ajira kwa wananchi, kimeboresha kipato cha
wananchi hususan wafugaji kupitia upatikanaji wa soko la uhakika la
ngozi, na kuchochea mnyororo wa thamani wa sekta ya mifugo nchini.
“Kiwanda
chetu kinazalisha bidhaa zenye ubora mkubwa, kimeongeza ajira kwa
wananchi na kimefungua soko la uhakika la ngozi kwa wafugaji wetu, jambo
linalonufaisha jamii na taifa kwa ujumla,” alisema Bw. Magambo.