-Asisitiza Ushirikiano wa Kimataifa, Majadiliano ya Kimkakati na mbinu za pamoja kukabiliana na changamoto za kidunia.

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Stephen Mbundi amekutana na Washiriki wa Kozi ya 14 kutoka Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC) waliotembelea Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mtumba jijini Dodoma kwa ziara ya Mafunzo.

Akizungumza katika kikao na wanachuo hao Mhe. Balozi Mbundi alieleza kufurahishwa kwake na ziara hiyo ambayo inawapatia mafunzo kwa vitendo wanachuo hao na kusisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa, majadiliano ya kimkakati, na mbinu za pamoja kama nyenzo za kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazoikabili dunia.

Alisema kuwa mazingira ya usalama duniani yanabadilika kutokana na changamoto mbalimbali kama za mivutano ya kisiasa kati ya mataifa, uhalifu wa kuvuka mipaka, ugaidi, vitisho vya mtandao, mabadiliko ya tabianchi na za kiuchumi.

Aliongeza kuwa ni matumaini yake ziara hiyo itachangia kuimarisha uelewa wa washiriki kuhusu uhusiano kati ya diplomasia, usalama wa taifa na ushirikiano wa kimataifa na kuimarisha ushirikiano kati ya Wizara ya Mambop ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Chuo hicho.

Katika kikao hicho Balozi Mbundi alielezea kwa ufupi historia, majukumu, dira na dhamira ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki katika kusimamia sera ya mambo ya nje, kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia, na kukuza ushirikiano wa kikanda kupitia taasisi kama Jumuiya ya Afrika Mashariki na Umoja wa Afrika.

Naye Mwakilishi wa Mkuu wa Chuo cha NDC, Brigedia Jenerali Selemani Bakari Gwaya alieleza kuridhishwa kwao na mchango wa Wizara katika kufanikisha kozi mbalimbali zinazotolewa na chuo hicho ambao unakiwezesha kukua kimataifa na kuaminika kama taasisi ya kimkakati.

Amepongeza juhudi za Wizara kwa kuendelea kutekeleza diplomasia ya uchumi kwa weledi na Vitendo licha ya changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika siasa za kimataifa.

Wanachuo 72 wa Kozi ya 14 ya NDC kutoka nchi 17 za Tanzania, Bangladesh, Botswana, Burundi, Misri, Ethiopia,India, Kenya, Malawi, Namibia, Nigeria, Rwanda, Sierra Leone, Afrika Kusini, Uganda, Zambia na Zimbawe waliambatana na Wakufunzi na Viongozi wao walifika Wizarani kwa lengo la kujifunza jinsi Wizara inavyotekeleza majukumu yake.












Na Mwandishi Wetu, Songea na Iringa

Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imewakutanisha wazabuni na Taasisi Nunuzi wa mikoa ya Ruvuma, Iringa na Njombe na kuwajengea uwezo kuhusu Moduli ya kupokea na kushughulikia Malalamiko na rufaa kwenye mfumo wa NeST kwa lengo la kuimarisha utendaji kazi. 

Mafunzo hayo yamefanyika kwa nyakati tofauti katika miji ya Songea na Iringa yamewahusisha washiriki 380 ambao ni wazabuni, wataalamu wa ununuzi, sheria, Tehama pamoja na makundi maalum yakiwemo wanawake, vijana, wazee na watu wenye mahitaji maalum pamoja na mafundi wa ndani.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando amesema mafunzo hayo yamekuwa yakitolewa na PPAA kwa kushirikiana na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) kwa lengo la kuwajengea uwezo wazabuni na Taasisi Nunuzi ili kuwapa ufanisi zaidi wakati wa utekelezaji wa majukumu yao, hususan katika kushughulikia malalamiko na migogoro itokanayo katika michakato ya ununuzi wa Umma. 

“Mafunzo haya yanalenga kuimarisha utendaji kazi wenu, kuhakikisha ufanisi, kuongeza uelewa wa matumizi ya Moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika wa Mfumo wa Ununuzi wa Umma kwa Njia ya Kielektroniki (NeST),” amesema Bw. Sando 

Bw. Sando ameongeza kuwa, katika kutimiza azma ya Serikali mafunzo yamewashirikisha vijana, wanawake na makundi maalum katika ununuzi wa umma ili kuwawezesha kupata elimu kuhusu ununuzi wa Umma hususan katika michakato ya ununuzi na kuhakikisha kuwa wanaisaidia Serikali kupata thamani halisi ya fedha katika miradi ya kimkakati yenye tija kwa Taifa.  

Pamoja na mambo mengine, Bw. Sando amewasihi washiriki kutumia mafunzo hayo kujifunza namna moduli ya kuwasilisha malalamiko na rufaa inavyofanya kazi katika Mfumo wa NeST kwani inatoa njia rahisi, ya haraka na yenye uwazi kwa wadau wote kushiriki katika mchakato wa ushughulikiaji wa malalamiko yanayotokana na michakato ya zabuni za umma. 

“Matumizi ya moduli yameongeza ufanisi katika usimamizi wa rufaa, kupunguza muda wa kushughulikia mashauri, na kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika utoaji wa haki, kuokoa muda na kupunguza gharama zinazohusiana na usuluhishi wa migogoro ya ununuzi,” ameongeza Bw. Sando

Kwa upande wake Meneja wa Usimamizi wa Rufaa na Sheria (PPAA), Bi. Florida Mapunda amesema kuwa mafunzo hayo yamelenga kutoa elimu kwa wadau wa ununuzi wa Umma kuhusu taratibu za uwasilishaji na ushughulikiaji wa malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST. 

“PPAA kwa kushirikiana na PPRA tumejenga moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko katika mfumo wa NeST ili kuwasaidia wadau wa ununuzi wa umma (Wazabuni na Taasisi za Umma) kuwasilisha malalamiko na rufaa kwa ufanisi zaidi kupitia mtandao,” amesema Bi. Mapunda.Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando akifungua mafunzo kuhusu Moduli ya kupokea na kushughulikia Malalamiko na rufaa kwenye mfumo wa NeST kwa wazabuni na Taasisi Nunuzi wa Mkoa wa Ruvuma. Kushoto ni Meneja wa Usimamizi wa Rufaa na Sheria (PPAA), Bi. Florida Mapunda na kulia ni Mkuu wa Sehemu ya Sheria PPAA, Bi. Agnes Sayi. Meneja wa Usimamizi wa Rufaa na Sheria (PPAA), Bi. Florida Mapunda akiwasilisha mada kuhusu uwasilishaji na ushughulikiaji wa malalamiko katika mfumo wa NeST kwa wazabuni na Taasisi Nunuzi walioshiriki mafunzo mkoani Ruvuma.
 Afisa Sheria kutoka PPAA, Bw. Venance Mkonongo akiwasilisha mada kuhusu uwasilishaji na ushughulikiaji wa malalamiko na rufaa katika ununuzi wa umma kwa wazabuni na Taasisi Nunuzi walioshiriki mafunzo mkoani Ruvuma.
Mkuu wa Sehemu ya Sheria PPAA, Bi. Agnes Sayi akiwasilisha mada kwa washiriki walioshiriki mafunzo kuhusu Moduli ya kupokea na kushughulikia Malalamiko na rufaa kwenye mfumo wa NeST kwa wazabuni na Taasisi Nunuzi wa Mikoa ya Iringa na Njombe. 
Mwezeshaji kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Bw. Daniel Kimaro akiwasilisha kuhusu utoaji wa tuzo, uandaaji, upekuzi, na utiaji saini wa mkataba kwa wazabuni na Taasisi Nunuzi wa Mikoa ya Iringa na Njombe. Sehemu ya wazabuni na Taasisi Nunuzi walioshiriki mafunzo kutoka Mikoa ya Iringa na Njombe

Viongozi wa PPAA wakiongozwa na Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando, katika picha ya pamoja na Kundi la wazabuni wenye mahiotaji maalum. Wengine pichani ni Meneja wa Usimamizi wa Rufaa na Sheria (PPAA), Bi. Florida Mapunda (kushoto)na kulia ni Mkuu wa Sehemu ya Sheria PPAA, Bi. Agnes Sayi.

 



Na Said Mwishehe,Michuzi TV-Njombe

MRADI wa kuzalisha umeme wa maji wa Lupali uliopo Kijiji cha Boimanda wilayani Njombe wenye uwezo wa kuzalisha kilowati 317 unaosimamiwa na Shirika la Benedictine Sisters of St. Gertrud Convent unatarajiwa kukamilika na kuingizwa katika gridi ya Taifa ndani ya miezi mitatu kuanzia sasa.

Katika kuufanikisha mradi huo Serikali kupitia Wakala wa Umeme Vijijini(REA) imetoa ruzuku ya fedha Sh.bilioni 5.4 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu mbalimbali ya mradi huo unaokwenda kuhudumia wananchi wa Wilaya hiyo.

Akizungumza leo Machi 11,2026 mbele ya Jukwaa la Wahariri Tanzania(TEF)wanaotembelea miradi ya REA ,Kaimu Meneja Usaidizi wa Kiufundi kwa Waendelezaji wa Miradi wa REA Mhandisi Emmanuel Yessaya amesema mradi huo ni sehemu ya uwekezaji wa sekta binafsi katika uzalishaji wa umeme utakaoingizwa katika gridi ya taifa kupitia Mkoa wa Njombe.

Amefafanua tayari miundombinu ya mradi huo imekamilika na kwasasa upo hatua za mwisho kuanza uzalishaji umeme ambao utaunganishwa katika gridi ya Taifa huku akifafanua mradi huo ulibuniwa na Shirika la Benedictine Sisters of St. Gertrud Convent kutokana na kukosekana umeme katika shirika hilo na vijijini jirani ingawa tayari REA imeshapeleka umeme.

“Miradi kama hii inasaidia kuongeza upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa wananchi na kuchochea shughuli za kiuchumi.Nitoe rai kwa wawekezaji kutumia fursa zilizopo kwenye maeneo yenye vyanzo vya maji kuanzisha miradi ya kuzalisha umeme.”

Amefafanua katika mikoa ya Njombe, Iringa na Ruvuma kuna vyanzo vya maji vingi ambavyo vinaweza kutumika kwa ajili ya miradi ya kuzalisha umeme,hivyo ni wakati muafaka kuchangamkia fursa na REA ipo tayari kushirikiana nao.

Kwa upande wake, Mratibu wa Mradi huo, Sister Imaculatha Mlowe kutoka Shirika la Benedictine Sisters of St. Gertrud Convent ameeleza ruzuku iliyotolewa na REA imesaidiakukamilisha ujenzi wa miundombinu ya mradi ikiwemo ujenzi wa intake weir, jengo la kuzalishia umeme,uwekaji wa mabomba ya kusafirisha maji, pamoja na kazi nyingine za ujenzi.

Pia amesema fedha iliyotolewa na REA imesaidia kugharamia tafiti za awali za mradi, ujenzi wa njia kuu za kusafirisha umeme za msongo wa kilovoti 11 zenye urefu wa kilomita 23.48 na njia ndogo za kusambaza umeme kwa watumiaji zenye urefu wa kilomita 30.61.

“Miundombinu ya kusafirisha na kusambaza umeme imeshakamilika na itaunganishwa gridi ya taifa kupitia TANESCO kwani tayari imefika katika kijiji jirani cha Kitulila.

“Hadi sasa wananchi zaidi ya 212 wa Kijiji cha Boimanda wameunganishwa na kupata huduma ya umeme kupitia gridi ya TANESCO wakati wananchi 366 wa Kijiji cha Matola wakipata umeme kupitia mradi wa zamani wa Lupali.”

Wakati huo huo Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Deodatus Balile, amesema mradi mradi huo unaonesha namna ushirikiano kati ya serikali na sekta binafsi unavyoweza kusaidia kuharakisha maendeleo ya kiuchumi nchini.

“Uzalishaji umeme ni moja ya vigezo muhimu vya maendeleo ya taifa kwani miradi ya aina hiyo itasaidia Tanzania kufikia malengo ya kuongeza uzalishaji wa umeme kutoka megawati 4,031 za sasa hadi kufikia megawati 8,000 ifikapo mwaka 2030.”











Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Machi 11, 2026 ameongoza Kikao cha kujadili Mapendekezo ya kufanya Maboresho ya Sheria ya Mapato ya baadhi ya Mifuko kilichofanyika kwenye ukumbi wa Waziri Mkuu, Bungeni jijini Dodoma, Machi 11, 2026.

Baadhi ya viongozi walioshiriki katika Kikao hicho ni pamoja na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, William Lukuvi, Waziri wa Ujenzi Abdallah Ulega, Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar, Waziri wa Madini, Anthony Mavunde na Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi.

Wengine ni Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Wanu Hafidh Ameir, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu- Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Ummy Nderiananga, Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Dkt. Jim Yonaz na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha Dkt. Natu El - maamry.









Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi, Ndg. Asha-Rose Migiro,leo tarehe 11 Machi 2026 amefanya mazungumzo jijini Dodoma na Balozi Parfait Onanga-Anyanga, Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Umoja wa Afrika na Mkuu wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa iliyopo Addis Ababa (UNOAU).

Balozi Onanga-Anyanga yupo nchini Tanzania kwa nafasi yake kama Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Mhe.António Guterres.

Kikao hicho ni sehemu ya mashauriano ya Mjumbe huyo na wadau mbalimbali wa kitaifa kwa lengo la kubadilishana mawazo kuhusu mustakabali wa kisiasa kufuatia Uchaguzi Mkuu wa tarehe 29 Oktoba, 2025, pamoja na juhudi pana za kuimarisha amani, demokrasia na mshikamano wa kitaifa nchini Tanzania.

Katika mazungumzo hayo, Ndg. Asha-Rose Migiro alisisitiza dhamira ya muda mrefu ya Tanzania katika kuendeleza utawala wa kidemokrasia, ushiriki wa kisiasa kwa njia ya amani na kuheshimu utawala wa sheria.

Alibainisha kuwa Tanzania inaendelea kuongozwa na misingi ya Mkataba wa Umoja wa Afrika wa Demokrasia, Uchaguzi na Utawala Bora, pamoja na viwango vya kimataifa vilivyowekwa katika Tamko la kimataifa la Haki za Binadamu na Mkataba wa kimatifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa.

Katibu Mkuu pia alieleza kuhusu mageuzi ya kisheria katika Tume ya Uchaguzi na taasisi nyingine yaliyofanyika kwa lengo la kuimarisha mfumo wa uchaguzi, ikiwa ni pamoja na kutungwa kwa sheria mpya za uchaguzi mwaka 2024 na hatua mbalimbali zilizolenga kuongeza uwazi, uwajibikaji na imani ya wananchi katika mchakato wa uchaguzi.

Mazungumzo hayo pia yaligusia matukio ya vurugu yaliyojitokeza katika baadhi ya maeneo nchini wakati na baada ya uchaguzi, ambayo yalisababisha upotevu wa maisha na uharibifu wa mali, ikiwemo mashambulizi dhidi ya ofisi za CCM. Ilibainishwa kuwa hatua stahiki zilichukuliwa kurejesha hali ya utulivu na amani nchini.

Pande zote mbili zilisisitiza umuhimu wa kuendelea kwa mazungumzo na maridhiano miongoni mwa wadau wa kitaifa. Hali kadhalika Katibu Mkuu wa CCM alimthibitishia Balozi Onanga-Anyanga kuwa Tanzania itaendeleza uhusiano wake na jumuiya ya kimataifa katika kuimarisha amani, usalama na maendeleo jumuishi.

CCM imepongeza ushirikiano madhubuti uliopo kati ya Tanzania na Umoja wa Mataifa na kuthibitisha dhamira yake ya kustawisha umoja wa kitaifa, utulivu na demokrasia katika Jamhuri ya Muungano ya Tanzania.






Na Mwandishi wetu - Dodoma 


Shirika la Maendeleo la Petroli Tanzania (TPDC) inaendelea kupanua miundombinu ya kusambaza gesi asilia kwa matumizi ya viwandani na majumbani katika Mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Lindi, Mtwara, na sasa mpango ni kufika Morogoro, Dodoma, Tanga, Kilimanjaro na Arusha.

Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi Mtendaji TPDC Mussa Makame akizungumza na Waandishi wa habari leo jijini Dodoma kutangaza Miradi ya Maendeleo na fursa za vijana kwa mwaka 2025/2026

 Makame amesema Vituo 14 vya kujaza gesi asilia (CNG) vimekamilika na vinahudumia vyombo vya usafiri ambapo lengo ni kuhamasisha matumizi ya gesi asilia, kupunguza utegemezi wa mafuta, na kuchangia katika kupunguza hewa ukaa. 

"TPDC inaunga mkono maono ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwa na asilimia 80 ya Watanzania wakitumia nishati safi ya kupikia ifikapo 2034"

Aidha Makame amesema hadi sasa, nyumba 2,515 zimeunganishwa na mtandao wa mabomba ya gesi asilia na tathmini ya kufikia maeneo mengine katika mikoa iliyofikiwa na bomba inaendelea ili kupanua wigo wa kuwafikia wateja.

Hata hivyo TPDC inashirikiana na Sekta binafsi kuanzisha miradi midogo ya gesi kimiminika (Mini-LNG) itakayowezesha kufikisha gesi asilia nchi nzima, na kuchangia katika maendeleo endelevu ya nchi.



 

Na Mwandishi wetu- Dodoma

Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali (GCLA) imefanikiwa kuwajengea uwezo vijana 8,086 katika uendeshaji wa shughuli zinazohusisha kemikali, na kuwasaidia kulinda afya zao na mazingira, Mafunzo hayo yamewezesha vijana kupata fursa za biashara katika usafirishaji wa kemikali na kuanzisha viwanda vidogo vidogo vya uzalishaji wa bidhaa za kemikali.

Dkt Fidelice Mafumiko Mkemia Mkuu wa Serikali ameyazungumza hayo leo jijini Dodoma katika Mkutano na Waandishi wa Habari kutangaza Miradi ya Maendeleo na fursa za vijana kwa mwaka 2025/2026

Mafumiko amesema Mamlaka imeendelea kuboresha miundombinu wezeshi, ikiwemo ujenzi wa majengo ya ofisi na maabara katika Ofisi ya Kanda ya Mashariki, jijini Dar es Salaam, wenye thamani ya Shilingi Bilioni 16.74, Ujenzi huo utaimarisha mazingira ya kufanyia kazi na utoaji huduma kwa wananchi.

 Pia amesema Mamlaka hiyo imekamilisha ujenzi wa nyumba za wafanyakazi katika mipaka ya Rusumo, Kabanga, Mutukula, Holili, na Namanga, wenye thamani ya Shilingi Bilioni 1.13, Juhudi hizo zinakusudia kuboresha mazingira ya kazi na makazi kwa wafanyakazi.

"Miradi hii imewasaidia vijana 260 kupata ajira, ikiwemo wataalam 27 na vibarua 233. Mamlaka inaendelea kuunga mkono sera za Serikali zinazohusiana na matumizi ya rasilimali za ndani (Local Content)"

Aidha Mafumiko amesema Mamlaka imeajili vijana 58 katika kazi za usafi wa mazingira na 38 katika ulinzi wa mali na majengo ya Mamlaka, hiyo inaonyesha jitihada za kuunda mazingira bora ya ajira kwa vijana.

Hata hivyo Katika kuimarisha matumizi ya TEHAMA, Mamlaka imeendelea kuboresha mifumo mbalimbali ya TEHAMA, na kukuza fursa kwa vijana katika sekta ya teknolojia.







Top News