Na ABDU MADENGE, WAF - DODOMA

Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala nchini limefuta usajili wa dawa ya Powaful Banana Medicine, kupiga marufuku uingizwaji na matumizi ya dawa ya Vitamax, pamoja na kuamuru kuondolewa sokoni kwa toleo namba MN1060 la dawa ya Joy.

Hatua hiyo imechukuliwa baada ya ukaguzi na vipimo vya maabara kubaini uwepo wa mchanganyiko wa kemikali hatari za kisasa na sumu kuvu kwenye bidhaa hizo kinyume cha sheria.

Hayo yamebainishwa na Mwenyekiti wa Baraza hilo, Prof. Nicolao Joseph Otieno, wakati wa mkutano na waandishi wa habari uliofanyika katika Ofisi za Wizara ya Afya Juni 05, 2026 Mkoani Dodoma ambapo ameeleza maamuzi hayo yanajiri kufuatia zoezi maalum la ufuatiliaji wa dawa sokoni (Post Market Surveillance) lililofanyika katika mwaka wa fedha wa 2025/2026, ambalo lilibaini ukiukwaji mkubwa wa Kanuni za Usimamizi wa Dawa za Tiba Asili kifungu cha 13(1)(a) na (b).

Prof. Otieno ameongeza kuwa Uchunguzi wa kimaabara umeonesha dawa ya Powaful Banana (inayotengenezwa na Powaful Products Company Ltd) na Vitamax (kutoka kampuni ya Superfood International ya Malaysia), ambazo zimekuwa zikitumika kuongeza nguvu za kiume, zimechakachuliwa kwa kuongezewa kemikali za kisasa za Sildenafil, Tadalafil, pamoja na dawa za maumivu aina ya Tramadol na Paracetamol.

“Tunaonya matumizi ya kemikali hizo bila usimamizi wa daktari yanaweza kusababisha magonjwa ya moyo, kufeli kwa ini na figo, shinikizo la damu, na hata vifo vya ghafla.” amesema Prof . Otieno.

Sambamba na hatua hizo, Baraza pia limebaini kuwa toleo namba MN1060 la dawa ya Joy (Usajili Na. TZ25TM0010) lina kiwango kikubwa cha sumu kuvu (mycotoxins) kinachoweza kusababisha saratani ya ini na uharibifu wa figo. Hali hii imetajwa kutokana na kutokuzingatiwa kwa viwango bora vya ukaushaji na uhifadhi wakati wa uzalishaji.

“Baraza tunatoa onyo kali kwa watengenezaji wote nchini ambao dawa zao zimebainika kuwa na mapungufu katika vifungashio, taarifa za lebo, ujazo, na maelezo ya dozi, tunawataka kufanya maboresho ya haraka kulingana na vigezo vya usajili kwa lengo la kulinda afya na usalama wa watumiaji.” amesema na kuongeza Prof. Otieno.



Na Beda Msimbe, TBN, aliyekuwa Urusi

IJUMAA, Juni 5, 2026, ilikuwa siku ya kihistoria na ya kipekee wakati Rais wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, alipokuwa akizungumza mbele ya viongozi wa dunia katika Jukwaa la Kimataifa la Uchumi la St. Petersburg (St. Petersburg International Economic Forum) na kuwasilisha hoja nzito zenye mashiko, akibeba sauti ya Watanzania wote huku akiweka wazi fursa zinazopatikana Tanzania pamoja na mwelekeo mpya wa nchi katika kujenga uchumi wa kisasa.

Jukwaa hilo lilikuwa sehemu muhimu ya ziara ya Rais Samia ambayo haikuwa tu ya kiitifaki, bali pia ya kufungua milango ya fursa za kiuchumi na kijamii.

Jinsi Rais Samia alivyopokewa na kukirimiwa nchini Urusi katika shughuli zote zilizomhusu, ilionesha taswira ya urafiki wa dhati na uelewano mkubwa kati yake na mwenyeji wake, Rais Vladimir Putin. Ziara hiyo ilifufua historia ya ushirikiano wa mataifa hayo mawili na kuweka wazi haja ya sasa ya kusaidiana katika kuleta ukombozi wa kiuchumi na ustawi wa jamii baada ya ukombozi wa kisiasa.

Akiwa katika jukwaa hilo la kiuchumi, hotuba ya Rais Samia iliwafanya washiriki wengi kutafakari kwa kina kutokana na hoja zake zilizojikita katika uchambuzi wa masuala ya dunia na umuhimu wa mabadiliko ya kimfumo katika uchumi wa kimataifa.

Rais Samia alitoa hoja yenye kuchokoza fikra aliposema kuwa ifikapo mwaka 2050, mtu mmoja kati ya wanne duniani atakuwa Mwafrika. Takwimu hiyo iliambatana na swali lenye uzito mkubwa: “Je, Afrika itastawi na kukua kwa masharti ya nani, na kwa modeli ipi ya uchumi?”

Swali hilo lilikuwa na mantiki kubwa katika kipindi ambacho siasa za kijiografia zimeendelea kuyumbisha ushirikiano wa kawaida wa kimataifa na kujaza mazingira ya masharti, ushindani na udhibiti wa kiuchumi unaozikandamiza nchi maskini.

Katika msingi huo wa kimantiki, Rais Samia alikuwa akiitaka dunia isiisitiri Afrika wala kuipangia mustakabali wake, bali itambue ukweli na kuiacha Afrika ijiamulie mambo yake yenyewe.

Mathalani, Afrika kwa sasa ina Ajenda 2063 pamoja na soko la pamoja la AfCFTA, lakini bado kuna mataifa yanayoendelea kuingilia masuala ya bara hilo na kuwagawa Waafrika ili waendelee kuonekana wanahitaji msaada wa kudumu katika kutatua changamoto zinazowakabili.

Rais Vladimir Putin aliunga mkono hoja hiyo, jambo lililoibua miguno ya ridhaa na vigelegele ukumbini. Kwa hakika, yapo mambo mengi ambayo Waafrika wanaweza kuyafanya wenyewe kwa manufaa yao na ya dunia kwa ujumla.

Mambo yaliyoguswa

Katika hotuba yake na ziara hiyo ya Urusi, Rais Samia aligusa masuala mengi muhimu. Hapa tunaweza kuangazia maeneo makubwa yaliyobebwa na ziara hiyo pamoja na namna makubaliano mbalimbali yalivyohitimishwa kwa mafanikio makubwa kwa Tanzania.

Ikumbukwe kuwa ziara ya Rais Samia, ambayo pia aliambatana na wafanyabiashara wa Tanzania, imeikumbusha dunia kuhusu mizizi imara ya kidiplomasia kati ya Tanzania na Urusi. Mahusiano hayo yana historia ndefu tangu miaka ya mwanzo ya uhuru, ambapo siku mbili tu baada ya Tanganyika kupata uhuru, Urusi ilituma salamu za pongezi; hali iliyojirudia pia wakati wa Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.

Mbele ya wawekezaji, Rais Samia alibainisha kuwa uchumi wa Tanzania unakua kwa kasi ya takribani asilimia sita, hali inayoiweka nchi miongoni mwa uchumi unaokua kwa kasi zaidi barani Afrika.

Aidha, alitangaza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kumfikisha kila Mtanzania kwenye kipato cha wastani cha dola za Marekani 7,000 huku akielezea kwa kina fursa mbalimbali za uwekezaji na biashara zilizopo nchini Tanzania.

Hotuba hiyo iliyopigiwa makofi mara kwa mara iliwavutia wawekezaji wengi wa Kirusi, ambapo sekta binafsi ya Urusi ilikiri kuwa Tanzania ni soko salama lenye utulivu wa kisiasa unaowezesha ukuaji wa mitaji na biashara.

Mbali na hayo, Rais Samia alieleza kuhusu mapinduzi makubwa ya miundombinu yanayoendelea nchini, hususan katika sekta ya reli na bandari. Katika mikutano ya pamoja na wafanyabiashara wa Tanzania na Urusi, alifafanua kwa kina kuhusu ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) inayounganisha Bandari ya Dar es Salaam na nchi za Rwanda, Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), pamoja na manufaa yake kwa ukanda mzima wa Afrika Mashariki na Kati.

Pia alieleza mpango wa miaka mitano wa kuipanua reli hiyo kuanzia mwaka 2026 hadi 2031 kuelekea Musoma na kuunganisha ukanda wa kusini kupitia Malawi hadi Msumbiji. Urusi, ikiwa na uzoefu mkubwa katika teknolojia ya reli na usafirishaji, ilionesha nia ya kutoa utaalamu wa kihandisi pamoja na mitambo ya kusaidia kuharakisha ujenzi wa reli hizo za kikanda.

Suala la maboresho ya mazingira ya uwekezaji na mfumo wa usajili wa saa 24 lilizua msisimko mkubwa miongoni mwa washiriki. Rais Samia alieleza kuwa uwekezaji umeongezeka kutoka dola bilioni tatu mwaka 2021 hadi dola bilioni 12 mwaka 2025 kutokana na maboresho ya mifumo ya uwekezaji, ikiwemo usajili wa kampuni unaokamilika ndani ya saa 24.

Kutokana na mafanikio hayo, Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) pamoja na taasisi za uwekezaji za Urusi zilisaini mikataba ya ushirikiano. Hatua hiyo ilipokelewa kwa furaha kubwa, ikionesha namna Tanzania ilivyojidhatiti kupunguza urasimu katika uwekezaji.

Aidha, miradi ya Eneo Maalum la Kiuchumi la Bagamoyo pamoja na Bandari ya Kimataifa ya Mizigo ya Mangapwani Zanzibar ilipewa kipaumbele na makampuni makubwa ya Urusi yanayojihusisha na usafirishaji wa baharini. Makampuni hayo yalikubali kutuma timu za wataalamu nchini Tanzania kufanya upembuzi yakinifu wa namna ya kuwekeza katika miradi hiyo.

Katika sekta ya madini, Rais Samia alisisitiza umuhimu wa kuongeza thamani ya madini ndani ya nchi. Tanzania ina utajiri mkubwa wa dhahabu, uranium, nickel, graphite, helium pamoja na madini adimu.

“Hatutaki tena kuuza malighafi pekee; tunataka viwanda vya usindikaji hapa nchini,” alisema Rais Samia.

Urusi, ambayo ni miongoni mwa mataifa yenye nguvu katika sekta ya madini, ilionesha utayari wa kushirikiana na Tanzania katika kujenga viwanda vya uchakataji na kuongeza thamani ya madini kabla ya kusafirishwa kwenda nje ya nchi.

Katika ziara hiyo, Rais Samia alidhihirisha wazi namna Tanzania ilivyo tayari kwa biashara, ubunifu na ushirikiano wa kimataifa unaolenga kukuza uchumi na ustawi wa wananchi wake.

Wakati Rais Samia akihitimisha hotuba yake katika jukwaa la St. Petersburg kwa kutoa shukrani za dhati kwa Rais Vladimir Putin kwa ukarimu wake, viongozi hao wawili walionesha tabasamu la furaha, ishara iliyotafsiriwa kama mwanzo mpya wa ushirikiano wa dhahabu kati ya Tanzania na Urusi.

Na Mwandishi Wetu

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete, amewataka wanafunzi wa sheria nchini kujenga taaluma zao katika misingi ya nidhamu, ubunifu na uzalendo ili waweze kushindana katika soko la ajira la kimataifa linalozidi kuwa na ushindani mkubwa.

Ridhiwani alitoa wito, wakati akizungumza katika hafla ya Siku ya Kazi na Taaluma ya Shule ya Sheria ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam iliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Alisema mafanikio ya taaluma katika dunia ya sasa hayawezi kupatikana bila wataalamu kuwa na uwezo wa kushindana nje ya mipaka ya nchi zao huku wakizingatia maadili ya kazi, hususan nidhamu, uzalendo na umahiri katika fani zao.

“Ni muhimu kwa wanafunzi wa sheria kuelewa kuwa taaluma zao zinahitaji siyo tu maarifa ya kisheria, bali pia maadili, nidhamu na uzalendo vitakavyowasaidia kuwa wataalamu wenye ushindani na mchango chanya kwa taifa,” alisema.

Aidha, Ridhiwani aliwaeleza wanafunzi hao kuhusu hatua zilizochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha sekta ya sheria na utoaji wa haki nchini.

Alisema serikali imeendelea kufanya mageuzi mbalimbali ikiwemo kuboresha mfumo wa haki, kuongeza matumizi ya teknolojia katika utoaji wa huduma za kisheria, kuwekeza katika miundombinu ya utoaji haki na kuhamasisha matumizi ya mifumo mbadala ya utatuzi wa migogoro.

Kwa mujibu wa Ridhiwani, maboresho hayo yanalenga kuwawezesha wanasheria na wasimamizi wa vyombo vya haki jinai kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi, sambamba na kujenga mazingira bora ya utoaji haki nchini.

Alisisitiza kuwa sekta imara ya sheria na haki ni nguzo muhimu katika kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii, huku wataalamu wa sheria wakibeba jukumu kubwa la kulinda maslahi ya taifa na kuimarisha utawala bora.






BODI ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) imeshiriki katika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Jukwaa la Wasimamizi wa Taaluma ya Ukaguzi Afrika (African Forum of Independent Accounting and Auditing Regulators (AFIAAR) wa mwaka 2026, unaofanyika mjini Port Louis, Mauritius kuanzia tarehe 2 hadi 5 Juni 2026.

Katika Mkutano huo, Mkurugenzi Mtendaji wa NBAA, CPA Prof. Siasa Mzenzi, alichaguliwa kuwa Makamu Mwenyekiti wa AFIAAR. Pamoja na Mkurugenzi Mtendaji, NBAA imewakilishwa na CPA Pius Maneno, Mkurugenzi Mtendaji Mstaafu wa NBAA na Makamu Mwenyekiti anayemaliza muda wake wa jukwaa hilo; CPA Winnington Makaka, Mkuu wa Sehemu ya Ubora wa Ukaguzi (AQR); pamoja na Magreth Kageya, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano cha NBAA.

Lengo la mkutano huo ni kuwakutanisha wasimamizi wa taaluma ya Uhasibu na Ukaguzi barani Afrika ili kujadili masuala mbalimbali yanayohusu taaluma hiyo, hususan hali ya ubora wa ukaguzi. Majadiliano hayo yanalenga kuimarisha ubora wa taarifa za ukaguzi wa makampuni, jambo litakalosaidia kukuza uchumi wa Afrika kwa kuongeza imani ya wawekezaji kupitia taarifa sahihi na za kuaminika za kifedha.

Akizungumza katika mkutano huo, Mkurugenzi Mtendaji wa NBAA na Makamu Mwenyekiti wa AFIAAR, CPA Prof. Siasa Mzenzi, alisema: “Mkutano huu ni muhimu kwa taasisi yetu na Tanzania kwa ujumla, kwani umetupatia fursa ya kujifunza na kubadilishana uzoefu kuhusu mbinu bora za usimamizi wa taaluma ya ukaguzi. Maarifa haya yatasaidia kuboresha ubora wa huduma za ukaguzi nchini na hivyo kuongeza uaminifu wa taarifa za kifedha zinazotolewa na taasisi na makampuni mbalimbali.”

Mkutano wa AFIAAR unawakutanisha wadau mbalimbali wa usimamizi wa taaluma ya ukaguzi kutoka nchi mbalimbali za Afrika kwa lengo la kuimarisha ushirikiano, kubadilishana uzoefu na kujadili mikakati ya kuendeleza ubora wa ukaguzi barani humo.











Mkurugenzi wa Kadama English Medium Primary School, Leticia Pastory, ameibuka mshindi wa Tuzo ya Mmiliki Bora wa Shule wa Kike Mkoa wa Geita kwa mwaka 2026. Tuzo hiyo imetolewa kwa kutambua mchango wake mkubwa kwenye sekta ya elimu.

Tuzo ilikabidhiwa rasmi Juni 6, 2026 na Mwenyekiti wa UWT Taifa na Mbunge, Mary Chatanda, kwenye Tamasha la Mwanamke wa Dhahabu 2026 lililofanyika Golden Social Hall, Geita. Tukio hilo liliandaliwa na Geita Women and Youth Foundation inayoongozwa na Mkurugenzi Cecylia Miraji.

Hafla hiyo muhimu ilihudhuriwa na Mkuu wa Mkoa Martine Shigela, Mbunge wa Geita Mjini Chacha Wambura, na Mkurugenzi wa Manispaa Yefred Myenzi.

Baada ya kupokea tuzo, Leticia alisema mafanikio hayo yanatokana na jitihada za miaka mingi za kuinua elimu Geita. Alibainisha kuwa Kadama imejijengea heshima kitaifa kutokana na matokeo mazuri na mazingira bora ya masomo.

Alikumbusha kuwa mwaka 2018 shule hiyo iliweka historia baada ya mwanafunzi wake kushika nafasi ya kwanza kitaifa na mwingine wa pili kwenye matokeo ya darasa la saba.

"Ni faraja kubwa. Tuzo hii inatupa nguvu kuendelea kutoa elimu bora na kuhamasisha wanawake wenzangu watumie nafasi zao kuleta mabadiliko," alisema Leticia.









Zaidi ya wanaushirika 2,000 wamepata mafunzo ya ushirika na maendeleo binafsi kupitia Jukwaa la Tano la Maendeleo ya Ushirika Mkoa wa Dodoma lililofanyika Juni 5 hadi 6, 2026 jijini Dodoma, likiwa na lengo la kuwakutanisha wadau wa ushirika kujadili mafanikio, changamoto na fursa za maendeleo katika sekta hiyo.

Akizungumza wakati wa kuwasilisha taarifa ya maendeleo ya ushirika mbele ya mgeni rasmi, Naibu Waziri wa Kilimo, Mhe. David Silinde, Mrajisi Msaidizi wa Vyama vya Ushirika Mkoa wa Dodoma, Joseph Chintika, Juni 6, 2026.

Amesema ushirika utaendelea kuwa na tija iwapo wanachama watazingatia uadilifu, utoaji wa huduma bila ubaguzi pamoja na kuhakikisha mazao yanayouzwa yanakuwa safi na yenye ubora, ikiwa ni moja ya nyenzo muhimu katika kuwasaidia wakulima kupata bei nzuri na kuongeza ushindani wa bidhaa zao katika soko.

Katika hatua nyingine, Chintika amesema matumizi ya mifumo ya kidijitali katika vyama vya ushirika mkoani Dodoma yameongezeka kutoka vyama 40 hadi 60, sawa na ongezeko la asilimia 23, hatua ambayo imechangiwa na juhudi za kuhamasisha matumizi ya teknolojia katika usimamizi wa shughuli za ushirika.

Aidha, amesema usajili wa wanachama umeongezeka kwa asilimia nne kutokana na mwamko unaoendelea kutolewa kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kujiunga na vyama vya ushirika.

Ametoa shukrani kwa Mrajisi Mkuu wa Vyama vya Ushirika nchini kwa mchango wake katika kuimarisha na kukuza sekta ya ushirika nchini, hali ambayo imewezesha vyama vingi kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wanachama.

Kwa mujibu wa Chintika, Mkoa wa Dodoma una jumla ya vyama vya ushirika 127 vinavyojumuisha SACCOS, vyama vya mazao na vyama vingine vya ushirika, vyenye jumla ya wanachama 22,228.

Amesema hadi sasa vyama 82 kati ya hivyo vimefikiwa na kupewa elimu mbalimbali za ushirika kwa lengo la kuongeza ufanisi, uwajibikaji na tija katika shughuli zao za kila siku.




Serikali imeziagiza Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA) na Soko la Bidhaa Tanzania (TMX) kuhakikisha mazao ya kimkakati yanayozalishwa na wanaushirika yanakusanywa na kuuzwa kupitia mfumo wa stakabadhi ghalani kwa vyama vya ushirika pekee, badala ya wanunuzi binafsi.

Maagizo hayo yametolewa na Naibu Waziri wa Kilimo, Mhe. David Silinde, wakati akifunga Jukwaa la Tano la Maendeleo ya Ushirika Mkoa wa Dodoma Juni 6, 2026.

Mhe. Silinde amesema mfumo wa ushirika umeendelea kuthibitika kuwanufaisha zaidi wakulima, hivyo ni muhimu kuhakikisha mazao ya kimkakati yanauzwa kupitia vyama vya ushirika ili kuongeza tija na manufaa kwa wazalishaji.

Aidha, amezitaka COPRA na TMX kutafuta njia mbadala za kuboresha bei za mazao kufuatia malalamiko ya wakulima kuhusu bei za kuanzia kwenye minada kuwa ndogo na kutokidhi matarajio yao, amesema taasisi hizo zinapaswa kuhakikisha wakulima wanapata bei nzuri na zenye kuridhisha ili kunufaika ipasavyo na uzalishaji wao.

Naibu Waziri huyo amesema Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya kisera na kisheria kwa lengo la kuimarisha sekta ya ushirika nchini, huku ikihakikisha wakulima wanazalisha mazao yenye ubora wa ushindani katika soko la ndani na la kimataifa.

Katika kuongeza upatikanaji wa mitaji, amezitaka benki hususan Benki ya Ushirika kutoa mikopo yenye riba nafuu kwa vyama vya ushirika na wanaushirika binafsi ili kuongeza uzalishaji na tija katika sekta ya kilimo.

Sambamba na hilo, ameitaka Shirika la Ukaguzi na Usimamizi wa Vyama vya Ushirika (COASCO) kuhakikisha vyama vyote vya ushirika vinakaguliwa kwa wakati, huku akiitaka Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC) kuongeza kasi ya usimamizi na ufuatiliaji wa vyama vya ushirika nchini.

Mhe. Silinde amesema ushirika ni nyenzo muhimu katika kukuza uchumi wa taifa, kuongeza ajira za kudumu na za muda mfupi pamoja na kuboresha maisha ya wananchi.

Aidha, ametoa onyo kwa baadhi ya wanaushirika wenye tabia ya kujinufaisha binafsi kwa gharama ya wanachama wengine kuacha mara moja vitendo hivyo, akieleza kuwa vinaweza kusababisha migogoro, chuki, wizi na kupoteza malengo ya msingi ya ushirika.

Amesisitiza kuwa ushirika una mchango mkubwa katika kuunganisha nguvu za pamoja, kulinda wakulima dhidi ya unyonyaji, kuchochea ubunifu na kuimarisha mafunzo ya pamoja kwa wanachama, jambo linalochangia maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.


WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali imejipanga kuanza ujenzi wa barabara ya Mafinga–Mgololo kwa kiwango cha lami katika mwaka wa fedha 2026/2027 huku ikiendelea kutekeleza miradi ya kuimarisha miundombinu ya umeme ili kuondoa changamoto ya kukatika kwa umeme katika Wilaya ya Mufindi.

Amesema hayo jana Jumamosi (Juni 6, 2026) alipokuwa akizungumza na kusikiliza kero za wananchi wa Halmashauri ya Mji wa Mafinga mkoani Iringa.

Dkt. Mwigulu alisema barabara ya Mafinga–Mgololo ni miongoni mwa miradi ambayo utekelezaji wake ulipungua kasi kutokana na Serikali kuelekeza nguvu katika kukamilisha miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo Mradi wa Kuzalisha Umeme wa Julius Nyerere (JNHPP), Reli ya Kisasa (SGR) na Daraja la Kigongo–Busisi.

“Nilikuwepo pale pale kwenye chungu, najua kona kona zile, najua ule ukoko utatoka wapi, fedha zije na barabara hii ianze kujengwa. Nitaisimamia na nitaifuatilia kwa sababu inaungana na ahadi za Mheshimiwa Rais na ahadi za Serikali kwa wananchi,” alisema.

Alisema Serikali imeanza utekelezaji wa mpango wa kufufua miradi ambayo mikataba yake ilishasainiwa pamoja na ile ambayo wakandarasi walikuwa bado hawajapewa malipo ya awali ili waweze kuingia maeneo ya kazi.

Kuhusu huduma ya maji, Dkt. Mwigulu alisema Serikali itaendelea kusimamia utekelezaji wa mradi wa maji wa miji 28 ambao unalenga kuongeza upatikanaji wa maji katika Mji wa Mafinga na maeneo ya jirani. Alisema mradi huo ni miongoni mwa miradi ambayo awali ilikumbwa na changamoto za upatikanaji wa fedha baada ya kusainiwa kabla ya fedha kupatikana, lakini sasa Serikali imeweka utaratibu wa kuhakikisha fedha za miradi ya maji zinapelekwa moja kwa moja kwenye mifuko ya maji ili kuharakisha utekelezaji wake.

“Maji ni jambo la lazima, maji ni maisha. Mradi huu ni miongoni mwa miradi nitakayofuatilia kwa karibu ili ukamilike na wananchi wa Mafinga wapate huduma ya maji ya uhakika,” alisema.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nishati, Salome Makamba alisema Serikali imetenga shilingi bilioni 3.9 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya umeme katika Wilaya ya Mufindi ikiwemo kutenganisha laini zinazohudumia viwanda na zile zinazohudumia matumizi ya majumbani.

Alisema Serikali pia inaendelea na ujenzi wa kituo cha kupoza umeme katika eneo la Kisada pamoja na kuimarisha mtandao wa usambazaji wa umeme ili kuongeza upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa wananchi na viwanda vya Mafinga.

Naye Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Dkt. Jafar Seif alisema Serikali kupitia Mradi wa TACTIC inaendelea kuboresha miundombinu ya Halmashauri ya Mji wa Mafinga ikiwemo ujenzi wa barabara za lami zenye urefu wa kilomita 11.8 pamoja na miundombinu ya soko la kisasa na stendi ya mabasi kwa lengo la kuboresha huduma za usafiri, biashara na kuchochea ukuaji wa uchumi wa mji huo.

Alisema miradi hiyo itatekelezwa kupitia awamu ya tatu ya Mradi wa TACTIC na itanufaisha wananchi wa Mafinga kwa kuboresha mazingira ya biashara, usafiri na utoaji wa huduma za kijamii.

Dkt. Seif pia alisema Serikali imeendelea kuimarisha huduma za afya katika Mji wa Mafinga ikiwemo kukamilisha mtambo wa kuzalisha hewa tiba (Oxygen Plant) ambao utahudumia Mkoa wa Iringa na maeneo mengine ya Nyanda za Juu Kusini. Alisema uwekezaji huo ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuimarisha huduma za matibabu ya dharura na kuhakikisha upatikanaji wa hewa tiba katika hospitali za umma.

Awali, Mbunge wa Mafinga Mjini, Dickson Lutevele aliiomba Serikali kuharakisha utekelezaji wa mradi wa barabara ya Mafinga–Mgololo, kukamilisha mradi wa maji wa miji 28, kuimarisha huduma ya umeme pamoja na kuharakisha utekelezaji wa miradi ya TACTIC kutokana na umuhimu wake katika kukuza shughuli za kiuchumi, viwanda na ustawi wa wananchi.





Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kinatarajia kuadhimisha Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu kuanzia Juni 9 hadi 11, 2026, katika Kampasi ya Mwalimu Julius Nyerere, huku Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, akitarajiwa kuwa mgeni rasmi.

Maadhimisho hayo yatakayowakutanisha watafiti, wabunifu, wanafunzi, sekta binafsi, taasisi za umma na wadau wa maendeleo, yanalenga kuonesha mchango wa utafiti na ubunifu katika kuharakisha maendeleo ya taifa na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Kaimu Naibu Makamu Mkuu wa Chuo anayeshughulikia Utafiti, Profesa Nelson Boniface, alisema maadhimisho ya mwaka huu yataongozwa na kaulimbiu isemayo: "Kutumia Utajiri wa Madini wa Tanzania katika Kukuza Nishati Jadidifu, Mageuzi ya Kidijitali na Usalama wa Jamii."

Alisema kaulimbiu hiyo imechaguliwa kutokana na umuhimu wa madini katika maendeleo ya teknolojia za kisasa ikiwemo Akili Mnemba (AI), vituo vya kuhifadhi taarifa (Data Centres), magari ya umeme na nishati jadidifu.

“Tunataka kuonesha namna Tanzania inaweza kutumia rasilimali zake za madini kuchochea mageuzi ya kidijitali, kuimarisha usalama wa nishati na kukuza maendeleo ya kijamii na kiuchumi,” alisema Profesa Boniface.

Aliongeza kuwa maadhimisho hayo yatahusisha maonesho ya tafiti na ubunifu, mawasilisho ya kitaaluma, makongamano pamoja na majadiliano ya ushirikiano wa kimkakati yatakayowawezesha washiriki kubadilishana maarifa na kujenga mitandao ya kitaaluma na kibiashara.

Kwa mujibu wa UDSM, maadhimisho hayo yatatoa nafasi kwa watafiti na wabunifu kuonesha suluhisho mbalimbali za kisayansi na kiteknolojia zinazolenga kukabiliana na changamoto za maendeleo nchini katika sekta za madini, nishati, kilimo, afya na uchumi wa kidijitali.

Profesa Boniface alisema chuo kinaendelea kutumia maadhimisho hayo kama jukwaa la kuunganisha taaluma, ubunifu na maendeleo ya taifa kwa kuwafikia wananchi, wawekezaji na wadau mbalimbali wa maendeleo.

"Utafiti na ubunifu ni msingi wa maendeleo endelevu. Tunawaalika Watanzania wote kushiriki katika Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu UDSM 2026 ili kujionea kazi na mafanikio ya watafiti na wabunifu wetu," alisema.


 


Na Mwandishi Wetu, Kagera
KATIBU Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi, amesema kuwa maendeleo na ukuaji wa biashara ya kaboni nchini yanapaswa kwenda sambamba na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, akisisitiza kuwa sekta hiyo ni miongoni mwa nyenzo muhimu zitakazochochea ukuaji wa uchumi, uhifadhi wa mazingira na ustawi wa wananchi katika kipindi cha miongo ijayo.

Dkt. Muyungi alitoa kauli hiyo leo mkoani Kagera wakati alipokutana na wadau wa biashara ya kaboni katika kikao kilichofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Katibu Tawala wa Mkoa wa Kagera. Kikao hicho kilihudhuriwa na viongozi wa serikali, wataalamu wa mazingira, wadau wa sekta binafsi pamoja na wawakilishi wa taasisi zinazojihusisha na biashara ya kaboni.

Akizungumza katika kikao hicho, Dkt. Muyungi alisema Serikali imeweka mkazo katika kuhakikisha kuwa biashara ya kaboni inasimamiwa kwa ufanisi ili iweze kutoa manufaa ya kiuchumi kwa wananchi huku ikiendelea kuimarisha juhudi za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Alieleza kuwa utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 unaotarajiwa kuanza Julai 1, 2026 unatoa nafasi kubwa kwa sekta mbalimbali, ikiwemo biashara ya kaboni, kuchangia katika kufikia malengo ya maendeleo ya taifa.

Alisema kuwa Tanzania imebarikiwa kuwa na rasilimali nyingi za asili, hususan misitu, ambayo inaweza kutumika kuzalisha mikopo ya kaboni (carbon credits) na hivyo kuongeza mapato kwa wananchi na taifa kwa ujumla. Aidha, alibainisha kuwa biashara ya kaboni imeendelea kuwa moja ya fursa mpya za kiuchumi duniani kutokana na kuongezeka kwa jitihada za kimataifa za kupunguza uzalishaji wa gesi joto zinazochangia mabadiliko ya tabianchi.

“Serikali inaendelea kuweka mazingira bora yatakayowezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika biashara ya kaboni ili waweze kunufaika na fursa zinazotokana na sekta hii. Tunahitaji kuhakikisha kuwa ukuaji wa sekta hii unaendana na malengo ya maendeleo ya taifa na matarajio yaliyowekwa katika Dira ya 2050,” alisema Dkt. Muyungi.

Katibu Mkuu huyo alisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya serikali, sekta binafsi na wananchi katika kuhakikisha kuwa biashara ya kaboni inaleta manufaa ya moja kwa moja kwa jamii zinazoshiriki katika shughuli za uhifadhi wa mazingira. Aliongeza kuwa elimu kwa umma kuhusu fursa za biashara ya kaboni ni muhimu ili wananchi waweze kuelewa thamani ya rasilimali walizonazo na namna ya kuzitumia kwa maendeleo endelevu.

Aidha, aliwataka wadau wa biashara ya kaboni kuzingatia sheria, kanuni na miongozo iliyowekwa na Serikali ili kuhakikisha kuwa shughuli zote zinazofanyika zinakuwa na uwazi, uwajibikaji na manufaa kwa pande zote zinazohusika.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa KADERES, Bw. Leonard Kachebonao, alisema kuwa taasisi hiyo imeendelea kupanua ushiriki wa wananchi katika biashara ya kaboni kupitia usajili wa wakulima wadogo na utoaji wa elimu kuhusu umuhimu wa uhifadhi wa mazingira kwa manufaa ya kiuchumi.

Alisema kuwa licha ya kampuni hiyo kuwa changa, tayari imefanikiwa kusajili wakulima wadogo wapatao 180,000 katika Mkoa wa Kagera, huku zoezi la usajili likiendelea katika wilaya mbalimbali za mkoa huo. Alieleza kuwa mwitikio wa wananchi umekuwa mkubwa kutokana na uelewa unaozidi kuongezeka kuhusu fursa zinazotokana na biashara ya kaboni.

“KADERES imeendelea kufanya kazi kwa karibu na jamii ili kuhakikisha wananchi wanashiriki kikamilifu katika miradi ya kaboni. Hadi sasa tumefanikiwa kusajili wakulima 180,000 na bado tunaendelea na zoezi hilo katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Kagera,” alisema Bw. Kachebonao.

Alifafanua kuwa kwa sasa shughuli za kampuni hiyo zinafanyika katika karibu wilaya zote za Mkoa wa Kagera isipokuwa Manispaa ya Bukoba, ambapo maandalizi ya kuanza utekelezaji wa shughuli hizo yanaendelea. Aliongeza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanapata nafasi ya kushiriki na kunufaika na biashara ya kaboni.

Mbali na Mkoa wa Kagera, Bw. Kachebonao alisema KADERES imejipanga kupanua shughuli zake katika maeneo mengine ya nchi, ikiwemo mikoa ya Morogoro na Pwani, ili kuongeza ushiriki wa wananchi katika miradi ya uhifadhi wa mazingira inayozalisha mikopo ya kaboni.

Alisema kuwa upanuzi huo utasaidia kuongeza mchango wa biashara ya kaboni katika maendeleo ya kiuchumi ya wananchi na taifa kwa ujumla, huku ukiimarisha juhudi za uhifadhi wa mazingira na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Kikao hicho ni sehemu ya juhudi za Serikali na wadau mbalimbali za kuendelea kuhamasisha ushiriki wa wananchi katika biashara ya kaboni, ambayo imeendelea kupata umuhimu mkubwa duniani kama moja ya suluhisho la kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi na kuchochea maendeleo endelevu.


Kampuni ya Mixx imejivunia kuendelea kuongezeka kwa idadi ya wateja wake pamoja na matumizi ya huduma zake za kifedha kidijitali kufuatia mwitikio mkubwa wa Watanzania katika kampeni ya “Kila Muamala ni Bao la Ushindi”, inayofanyika kwa ushirikiano na kampuni ya Hisense.

Akizungumza wakati wa droo ya pili ya kampeni hiyo, Mkurugenzi wa Biashara wa Mixx, James Sumari, amesema kampeni hiyo imekuwa kichocheo muhimu katika kuhamasisha matumizi ya njia rasmi za malipo ya kidijitali, huku idadi ya watumiaji wa huduma za Mixx ikiendelea kuongezeka nchini.

Sumari amesema moja ya mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kipindi hicho ni kuongezeka kwa matumizi ya Mixx Super App, ambayo watanzania zaidi ya milioni moja wanatumia App hiyo. Amesema hatua hiyo inaonesha imani kubwa ya Watanzania katika huduma za kidijitali na mchango wake katika kurahisisha miamala ya kifedha.

Ameeleza kuwa matumizi ya huduma za kidijitali kama Mixx yanasaidia kuimarisha usalama wa fedha za watumiaji, kupunguza utegemezi wa fedha taslimu na kuwezesha ufuatiliaji wa matumizi ya kifedha kwa urahisi zaidi kwa watu binafsi na wafanyabiashara.

Kwa mujibu wake, huduma hizo pia zinachangia kujenga nidhamu ya matumizi ya fedha, kuongeza uwazi katika shughuli za biashara na kusaidia usimamizi bora wa mapato, jambo linalochochea ukuaji wa uchumi wa kidijitali nchini. Aliongeza pia siri ya kushindi ni katika Kampeni hiyo ni kutumia zaidi Mixx Super App, kufanya miamala mingi kidigitali, kutumia huduma za Mixx kama Lipa kwa Simu ili kujiweka katika nafasi nzuri ya kushinda.

Wakizungumza baada ya kupokea zawadi zao, baadhi ya washindi wa kampeni hiyo wamesema ushindi huo umewapa hamasa zaidi ya kuendelea kutumia huduma za Mixx katika shughuli zao za kila siku.

Mmoja wa washindi hao, Sabdiki Vike, amesema alipokea taarifa za ushindi wake kwa mshangao mkubwa kwani awali alidhani ni utani au jaribio la utapeli. Hata hivyo, baada ya kuwasiliana na kampuni na kufika katika makao makuu ya Mixx, alithibitisha kuwa alikuwa mshindi halali wa kampeni hiyo.

Amesema matumizi ya Mixx Super App yamemrahisishia kupata huduma mbalimbali za kifedha katika sehemu moja na kufanya miamala kwa haraka na kwa urahisi, jambo ambalo limemfanya kuwa mtumiaji wa mara kwa mara wa huduma hiyo.

Kwa upande wake, Benson Benjamin amesema Mixx imekuwa msaada mkubwa katika kufanya miamala yake kwa usalama na urahisi zaidi. Ameeleza kuwa tangu kuanza kwa kampeni hiyo ameongeza matumizi ya huduma za Mixx, hali ambayo anaamini imechangia ushindi wake.

Benjamin ameongeza kuwa anatamani kushinda zawadi kubwa ya safari ya kwenda Mexico kushuhudia michuano ya Kombe la Dunia, jambo ambalo limemhamasisha kuendelea kutumia huduma za Mixx ili kuongeza nafasi ya kushinda.

Jumla ya washindi 20 walipatikana katika droo hiyo, wakitoka katika mikoa mbalimbali ikiwemo Dar es Salaam, Zanzibar, Arusha na maeneo mengine ya nchi. Mbali na washindi wa fedha taslimu wa shilingi milioni moja moja kila siku, baadhi yao pia walijishindia vifaa mbalimbali vya nyumbani kutoka Hisense, ikiwemo televisheni ya inchi 55, spika na jokofu, baada ya kutumia huduma za Mixx kufanya miamala.

Lengo la pili la Kampeni ya “Kila Muamala ni Bao la Ushindi” inalenga kuhamasisha matumizi ya huduma za kifedha kidijitali huku ikiwazawadia wateja wanaofanya miamala kupitia Mixx. Kampeni hiyo inaendelea kuwa sehemu ya juhudi za kukuza ujumuishaji wa kifedha na kuharakisha matumizi ya teknolojia katika huduma za kifedha nchini.

Mkurugenzi wa Biashara wa Mixx, James Sumari (katikati), akisherehekea pamoja na washindi wa kampeni ya Kila Muamala ni Bao la Ushindi, Sabdiki Vike (kulia) na Benson Mbile (kushoto), baada ya kila mmoja kujishindia Shilingi milioni 1 katika droo ya pili ya kampeni hiyo. Kampeni inalenga kuhamasisha matumizi ya huduma za kifedha kidijitali huku ikiwazawadia wateja wanaotumia huduma za Mixx.



HAKUNA haja ya kuwa na mamilioni ili kufurahia burudani ya kimataifa. Meridianbet imekuletea Leprechaun Wish, mchezo wa kasino unaokupeleka moja kwa moja kwenye ulimwengu wa Ireland uliojaa bahati, rangi na zawadi kubwa. Leo inaweza kuwa siku yako ya kung'ara.

Ndani ya mchezo huu utakutana na alama za kuvutia kama chungu cha dhahabu, sarafu za bahati, vito vya kifalme na kofia za kichawi. Kila mzunguko una msisimko wake na kila raundi inaweza kuwa mwanzo wa ushindi mkubwa.

Vilevile, meridianbet wana michezo mingi ya kasino mtandaoni na mechi za kimataifa za kubashiri zenye ushindani mkubwa wa odds. Jiunge leo kwa kutembelea tovuti ya MERIDIANBET au piga *149*10# kisha uanze safari yako ya ushindi.

Mistari 20 ya kubashiri inamaanisha nafasi nyingi zaidi za kujaribu bahati yako. Kadri unavyoendelea kucheza, ndivyo unavyoongeza nafasi ya kukutana na zawadi zinazoweza kubadilisha siku yako.

Kwa wale wasiopenda kusubiri, bonasi ya kununua imewekwa maalum kukupa nafasi ya kuingia moja kwa moja kwenye mizunguko yenye fursa kubwa za ushindi. Ni njia ya haraka ya kuongeza msisimko wa mchezo.

Ingia Meridianbet sasa ucheze Leprechaun Wish. Furahia burudani ya kipekee, tafuta bahati yako na ujaribu kufikia jackpot inayosubiri washindi wapya kila siku.

ZIMEBAKIA siku chache tuu kuelekea michuno mikubwa ya Kombe la Dunia Ulaya, ambapo wachezaji kutoka Mataifa mbalimbali wamejiandaa kufanya vyema. Meridianbet inakueletea wachezaji ambao wanaweza kuondoka na kiatu cha ufungaji bora.

Nafasi ya kwanza inaenda kwa Kylian Mbappe amnaye ni raia kutoka Ufaransa na anayekipiga pale Real Madrid. Mbappe atakuwa tayari kuongoza safu ya ushambuliaji chini ya kocha mkuu Didier Deschamps huku mchezaji huyo akiwa tayari ana uzoefu mkubwa kwenye mashindano haya akiwa amefunga mabao mengi kwenye mashindano haya.

Pia Ufaransa ni moja ya timu ambazo zinapewa nafasi kubw ayakufanya vyema kwenye mashindano hay hivyo, Kylian akisaidiana na wenzake kina Dembele, Doure, Olise na wengine anaweza akachukua kiatua hiko huku Meridianbet wakimpa ODDS 7.00. Je Mbappe ataondoka kinara wa ufungaji bora?. Jisajili hapa.

Mpunga mkubw a upo kwenye michezo ya kasino ya mtandaoni kama vile Keno, Aviator, Poker, Roullette, Wild Icy Fruits, Super Heli na mingine kibao. Jiunge leo kwa kutembelea tovuti ya meridianbet.co.tz au piga *149*10# kisha uanze safari yako ya ushindi.

Kutoka kule Uingereza mshambuliaji wa Bayern Munchen Harry Kane ndiye anayepewa nafasi kubwa ya kuondoka na kiatua hicho cha ufungaji bora kwenye Kombe hili la Dunia akiwa na ODDS 8.00. Akiwa na timu ya Taifa ya Uingereza Kane ni moja ya washambuliaji hatari sana kutokana na uwezo wake wa kupachika mabao.

Tayari akiwa na Bayern msimu huu amefunga mabao 61 hivyo kuwa kwake fiti kutampa nafasi kubwa ya kufanya vyema chini ya Thomas Tuchel. Mchezaji huyo pia ana uzoefu na michuano hii kwani tayari alishapachika mabao mengi kwenye michuano hii na mpaka sasa yeye ndiye kinara wa ufungaji bora Uingereza akiwa na mabao 78. Suka jamvi lako kwa Kane sasa.

Pia vilevile Lionel Messi ambaye ni Muargentina na mabingwa watetezi wa Kombe hili pia anapewa nafasi ya 3 kuchukua kiatua cha ufungaji bora msimu huu. Kwenye Kombe la Dunia la 2022 Messi alichukua tuzo ya mchezaji bora wa mashindano kutokana na ubora ambao alionesha kwenye mashindano hayo.

Nahodha huyo wa Argentina anapewa nafasi hiyo kutokana na kuwa timu yao inapewa pia nafasi kubwa ya kufanya vizuri lakini pia uwezo wa wachezaji kama Lautaro, Julian Alvarez, De Paul nawengine kunampa Messi nafasi kubwa ya kufunga ambao huku yeye pia akiwa ni mtengenezaji wa maboa hayo. ODDS za Messi kuchukua tuzo hiyo ni 13. Je wewe nafasi hiyo ya kuchukua kiatu bora unampa nani?. Beti hapa.

Halikadhalika naye Erling Haaland kutoka Norway anapewa nafasi kubwa ya kuchukua tuzo hiyo akiwa na timu yao ambayo mwaka huu imefuzu kucheza Kombe la Dunia baada ya miaka mingi sana. Haaland ameendelea kuonesha ubora wake akiwa na timu yake ya Manchester City baada ya kuchukua kiatua cha ufungaji kwenye ligi kuu ya Uingereza.

Timu ya Taifa ya Norway ina wachezaji wenye vipaji vikubwa sana wakiwemo Odegaard, Solorth, na wengine wengi ambao wana vipaji vikubwa. 15 ndio ODDS ambazo Haaland amepewa kuwa mfungaji bora wa michuano hii. Ingia na ujisajili sasa.

Nafasi ya 5 inaenda kwa Lamine Yamal ambaye ni Mhisapania na anapewa nafasi kubwa ya kuondoka na kiatu cha ufungaji bora. Hispania ni moja ya timu ambayo inapewa nafasi kubwa ya kufanya vyema kwenye michuano hii baada ya kuchukua taji la Euro.

Ukubwa na ubora wa wachezaji ambao wanao chini ya kocha mkuu Luis de la Fuente unawapa nafasi ya wao kufika mbali. Wana wachezaji kama Gavi, Pedri, Fabian Luiz, Dani Olno, Rodri, na wengine kibao wanaweza kufanya Lamine aondoke na kiatu. Lamine kuondoka na kiatua hicho ufungaji bora amepewa ODDS 15. Beti sasa.



 

 


Na Oscar Assenga,TANGA

SERIKALI imekipongeza Chama cha Washauri wa Wanafunzi wa Vyuo Vikuu Tanzania (TACOGA) kwa kuendelea kuandaa mafunzo yanayolenga kuimarisha uwezo wa kitaaluma na kiutendaji wa washauri wa wanafunzi, wanasihi na viongozi wa serikali za wanafunzi kutoka vyuo mbalimbali nchini.

Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo yaliyofanyika jijini Tanga,Mkurugezi wa Maendeleo ya Jinsia kutoka Wizara ya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wanawake na Makundi Maalumu Badru Abdnur alisema mafunzo hayo yamekuwa jukwaa muhimu la kuwajengea washiriki uwezo wa kukabiliana na changamoto zinazowakabili wanafunzi katika taasisi za elimu ya juu.
Alisema katika kipindi cha mafunzo hayo, washiriki walipata nafasi ya kujifunza, kubadilishana uzoefu na kujadili changamoto mbalimbali wanazokutana nazo katika utekelezaji wa majukumu yao, pamoja na kupata mbinu mpya zitakazowawezesha kuboresha huduma wanazozitoa kwa wanafunzi.

"Nawapongeza viongozi wa TACOGA kwa ubunifu na maono yao ya kuhakikisha mafunzo haya yanafanyika kila mwaka. Bila uongozi imara, kuandaa mafunzo ya aina hii si jambo rahisi," alisema.
Aliongeza kuwa hatua hiyo inaonesha utambuzi wa umuhimu wa maendeleo endelevu ya kitaaluma kwa watendaji wanaohusika na huduma za wanafunzi pamoja na viongozi wa serikali za wanafunzi.
Badru alibainisha kuwa mada zilizowasilishwa zimegusa maeneo nyeti yanayoathiri ustawi na maendeleo ya wanafunzi, ikiwemo afya ya akili, maadili, matumizi ya teknolojia na uongozi bora.

Alisema dunia ya sasa inabadilika kwa kasi kutokana na maendeleo ya kijamii, kiuchumi na kiteknolojia, hali inayowafanya vijana kuwa miongoni mwa makundi yanayoathirika zaidi na mabadiliko hayo.

"Vijana wanakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo afya ya akili, matumizi mabaya ya teknolojia, matumizi ya dawa za kulevya na mmomonyoko wa maadili. Hivyo, kuna haja ya kuendelea kuwajengea uwezo na kuwapa mwongozo sahihi ili wawe raia wema na wazalendo," alisema.
Aidha, aliwakumbusha washiriki kuwa serikali na jamii kwa ujumla zinategemea sana mchango wa washauri na wanasihi katika kuwajenga wanafunzi.


Alisema wazazi na walezi wana matumaini makubwa kwa maafisa hao kwa kuwa vijana wengi wanaojiunga na vyuo vikuu bado wana umri mdogo na wanahitaji mwongozo, uangalizi na malezi ya karibu.
Kwa mujibu wake, kutokana na nafasi hiyo muhimu, TACOGA ina wajibu mkubwa wa kuchangia mageuzi ya maendeleo ya taifa kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050.

Alitoa wito kwa chama hicho kuwekeza zaidi katika mifumo ya kiteknolojia ili kuendana na mazingira ya sasa ya kidijitali. Alisema ni muhimu kuanzisha mifumo ya kimtandao na programu za simu zitakazowezesha wanafunzi kupata huduma za ushauri kwa haraka na kwa urahisi bila kuathiri muda wao wa masomo.

Pia aliwataka kuendelea kujenga uwezo wa wanachama wao kupitia mafunzo endelevu ya saikolojia, unasihi na mbinu mpya za utoaji wa huduma ili kuwawezesha washauri na wanasihi kutoa suluhisho stahiki na la kisasa kwa changamoto zinazowakabili wanafunzi.
Vilevile, alisisitiza umuhimu wa kuimarisha viashiria vya kupima matokeo ya kazi zinazofanywa na TACOGA kwa kuwekeza katika tafiti ndogo ndogo za kutathmini kama huduma zinazotolewa zinaleta matokeo chanya katika ufaulu wa wanafunzi na maendeleo yao ya kijamii na kitaaluma.

Mgeni rasmi huyo pia alisisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya ofisi za washauri wa wanafunzi na madawati ya jinsia pamoja na vitengo vya kuzuia ukatili wa kijinsia katika vyuo vikuu. Alisema kuna muunganiko mkubwa wa majukumu kati ya taasisi hizo, hivyo ushirikiano ukiimarishwa utasaidia kupunguza mzigo wa kazi na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wanafunzi.

Alisema maarifa na stadi zilizopatikana kupitia mafunzo hayo zinatarajiwa kuwafanya washiriki kuwa mabalozi wa mabadiliko katika taasisi zao na kuchangia kufikiwa kwa Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TACOGA, Sophia Nchimbi, alisema chama hicho kimeendelea kuandaa mafunzo hayo kwa lengo la kuwawezesha maafisa wa ofisi za washauri wa wanafunzi katika vyuo vikuu kutekeleza majukumu yao kwa weledi zaidi.

Alisema washiriki walipata mafunzo yaliyohusu nidhamu chanya, usimamizi wa tabia, unasihi, matumizi salama ya mitandao ya kijamii, afya ya akili, malezi ya wanafunzi, uongozi bora na usimamizi wa madawati ya jinsia katika vyuo vikuu.

"Mafunzo haya yanatusaidia kupata ufumbuzi wa changamoto mbalimbali tunazokutana nazo katika maeneo yetu ya kazi. Maarifa tunayopata yanatupa uwezo wa kuwahudumia wanafunzi kwa ufanisi zaidi," alisema Nchimbi.
Alisema mada kuhusu matumizi ya mitandao ya kijamii zimewawezesha washiriki kuelewa namna bora ya kuwaelekeza wanafunzi kutumia teknolojia kwa manufaa ya elimu badala ya matumizi yasiyofaa.

Nchimbi alisema pia washiriki walipata elimu kuhusu namna ya kusimamia madawati ya jinsia ili kuhakikisha wanafunzi wanaokumbana na changamoto mbalimbali wanapata msaada kwa wakati na kwa usahihi.

Aliongeza kuwa TACOGA imekuwa ikifanikiwa kuendesha mafunzo hayo kutokana na ushirikiano mkubwa wa wanachama na wadau mbalimbali wanaochangia maendeleo ya huduma za ushauri kwa wanafunzi.

Jumla ya washiriki 94 kutoka vyuo mbalimbali nchini walishiriki mafunzo hayo yaliyofanyika jijini Tanga.

Top News