Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amekutana na kufanya mazugumzo na Balozi wa India nchini Tanzania Mhe. Bashwadip Dey, mazungumzo yaliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 20 Februari 2026.

Mazungumzo hayo, yamelenga kuimarisha zaidi ushirikiano baina ya India na Tanzania katika sekta mbalimbali za kimkakati. Mahusiano kati ya nchi hizi mbili yamejikita katika sekta ya Afya, Maji, Elimu,Biashara na Uwekezaji pamoja masuala ya Ulinzi na Usalama.

Tanzania na India zina mahusiano mazuri ya kidiplomasia yaliyoanza baada ya Tanzania kupata uhuru ambapo India ilifungua Ubaozi wake mwaka 1961 na Tanzania kufungua Ubalozi wake nchini India mwaka 1962.

Mwaka 2023 mahusiano kati ya nchi hizi mbili yaliongezeka zaidi na kuwa mahusiano ya kimkakati kufuatia ziara rasmi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, aliyoifanya nchini India.

India imekuwa na mchango mkubwa katika miradi mbalimbali ya maji inayotekelezwa na Serikali pamoja na kutoa mchango mkubwa katika sekta ya Afya ikiwemo utoaji wa huduma za afya nchini, mafunzo pamoja na Vifaa Tiba.

India imekuwa mdau muhimu wa biashara nchini Tanzania ambapo hadi sasa inashika nafasi ya tatu duniani kwa kufanya biashara na Tanzania. Bidhaa ambazo Tanzania inauza zaidi nchini India ni pamoja na Korosho, karanga, mboga za jamii ya kunde, vito vya thamani na vito vya thamani, pamba; karafuu, chai, Ngozi, mbao na bidhaa za mbao.









Na Mwandishi Wetu

Watumiaji wa gesi ya kupikia wamepata nafuu baada ya Oryx Gas Tanzania kuzindua kampeni ya “Pishi la Kibabe” kwa Ramadhan na Kwaresma, itakayoshusha bei ya mtungi mpya wa kilo sita hadi Sh. 37,000 nchi nzima.

Akizungumza leo Februari 20,2026 jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi huo Meneja Masoko na Mauzo wa Oryx Gas Tanzania Shaban Fundi amesema huu ni mwezi wa kujitafakari ,kushirikiana ,kujitolea na zaidi ya yote kuunganisha watu wote.

“Ili kuunga mkono wateja wetu katika kipindi hiki maalum tunatoa bei ya promosheni kwenye mitungi yetu mipya ya kilo sita itauzwa kwa Sh.37000 nchi nzima hadi Zanzibar.”amesema Fundi

Pia amesema mbali ya kupunguza bei katika kipindi hiki cha Ramadhan na Kwaresma wateja wao watakaonunua au kujaza gesi kwenye maduka maalum ya Oryx na Mangi Shop watapokea zawadi ya futari papo kama ishara ya shukrani yao kwao.

Akizungumza kuhusu gharama za mtungi wa kilo sita amesema mpaka unafika nchini Tanzania gharama yake haipungui Sh.80,000 lakini Oryx katika soko mtungi huo unapatikana kwa Sh.40000 na kwa sasa tumetoa promosheni mpaka Sh.37000.

-“Hata hivyo tunaomba Serikali iendelee kuangalia katika maeneo mengine ili kuhakikisha kwamba gesi pamoja na mtungi bei yake inakuwa chini ili wananchi waweze kupata kwa bei nafuu.Kwafanya hivyo Oryx Gas kwa kushirikiana na Serikali tunaweza kufanikisha matumizi ya nishati safi kwa wananchi wengi zaidi.”

“Kuhusu gharama ukilinganisha mkaa na kuni bei yake iko juu zaidi ya nishati safi ya kupikia kwani kwa familia ya kawaida kwa siku moja inatumia kopo moja la mkaa ambalo linauzwa Sh.2000 hivyo kwa mwezi ni Sh.60,000 wakati mtungi wa gesi ya oryx wa kilo 6 ni Sh.40,000.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Oryx Gas Tanzania Benoit Araman amesema lengo la kampeni iliyozinduliwa kwa ajili ya Mfungo wa Mwezi wq Ramadhan na Kwaresma ni muendelezo wa kuhamasisha matumizi ya nishati safi nchini ikiwa ni kuunga mkono juhudi za Serikali za kuhimiza wananchi kutumia nishati safi ya kupikia.

“Oryx Gas lengo letu kubwa ni kuendelea kuhamasisha nishati safi ya kupikia na mimi na timu yangu tumejipanga vema kuhakikisha tunaendelea kufanya kampeni za kuwezesha wananchi kutumia nishati safi ya kupikia.Wakati huu wa Ramadhan na Kwaresma tunawatakia mfungo mwema lakini wakati huo huo tukihamasisha matumizi ya nishati safi.”

Wakati huo huo Mkuu wa Idara ya Mauzo ya Gesi kwa Ujumla Carloline Msokwa amesema kipindi hiki Waislamu na Wakristo wanaungana pamoja kuomba toba na ni kipindi ambacho familia zinakaa kufanya ibada na kuomba toba lakini pia ni wakati wa kupika chakula kizuri kwa ajili ya kufuturu.

“Kwahiyo Oryx Gas tumekuja na kampeni ya Pishi la kibabe ambapo familia zitakaa na kupika pamoja lakini pia Oryx tumetoa punguzo la bei ili kuwezesha wananchi kutumia gesi.Pia nitoe rai huu ni wakati wa Watanzania kuwa wamoja na tuliombee taifa letu.”





Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Kanda ya Kati, Dodoma, Dkt. Japhet Nkangaga (kushoto), akipokea changamoto mbalimbali zinazowakabili wafugaji kutoka kwa muuzaji wa pembejeo za mifugo Manispaa ya Singida, Bi. Ester Munuo, tarehe 19 Februari 2026 mkoani Singida, wakati wa ziara ya uhamasishaji kwa wauzaji wa pembejeo za mifugo iliyolenga kutoa elimu kuhusu matumizi sahihi ya chanjo ya Matone (TEMEVAC) na taratibu za upatikanaji wa leseni za uuzaji wa viuatilifu vya rejareja na jumla.


*************


Na Daudi Nyingo – Singida

Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) imeendelea kuimarisha juhudi za kulinda afya ya mifugo nchini kwa kutoa elimu kwa wauzaji wa pembejeo za mifugo mkoani Singida kuhusu utoaji na matumizi sahihi ya chanjo za mifugo zinazozalishwa na taasisi hiyo. 

Zoezi hilo lililofanyika tarehe 19 na 20 Februari 2026 lililenga kuwajengea uwezo wauzaji wa pembejeo kama kiungo muhimu cha kuwafikia wafugaji, ili waweze kutoa elimu sahihi kuhusu utambuzi wa chanjo za TVLA, namna bora ya kuzitunza, matumizi sahihi na umuhimu wa kufuata taratibu za kitaalamu katika utoaji wa chanjo.

Akizungumza wakati wa kuhitimisha zoezi hilo tarehe 20 Februari 2026, Meneja wa TVLA Kanda ya Kati Dodoma, Dkt. Japhet Nkangaga, alisema kuwa ziara hiyo ililenga kutoa elimu kwa wauzaji wa pembejeo na wafugaji kuhusu matumizi sahihi ya chanjo ya Matone (TEMEVAC), ikiwemo namna bora ya kuzipokea, kuzihifadhi katika ubaridi unaostahili ili kudumisha ubora wake na kuhakikisha chanjo zinatumika kwa ufanisi unaokusudiwa.

“Tunasisitiza matumizi sahihi kuanzia hatua ya kufungua chupa ya chanjo. Kama imeandikwa kuwa na dozi 100, ni lazima itoe dozi 100. Endapo tundu litatobolewa kubwa, kunakuwa na uwezekano wa chanjo kutoka nyingi zaidi na kusababisha dozi zilizokusudiwa kutotimia,” alisema Dkt. Nkangaga.

Aliongeza kuwa elimu hiyo pia inahusisha matumizi sahihi ya chanjo baada ya kufunguliwa, akieleza kuwa kuku mmoja hupatiwa tone moja la chanjo na kurudiwa kuchanjwa baada ya miezi mitatu, utaratibu unaoendelea kwa mwaka mzima hadi kuku anapofikia hatua ya matumizi ya binadamu.

Baadhi ya wauzaji wa pembejeo za mifugo mkoani Singida wameibua changamoto ya upatikanaji wa chanjo mbalimbali, hali ambayo imekuwa ikiwalazimu wakati mwingine kupata chanjo kutoka vyanzo visivyo na uhakika. Wameshauri TVLA kuimarisha upatikanaji wa chanjo ili kuhakikisha wauzaji na wafugaji wanapata bidhaa salama, zenye ubora na kutoka katika vyanzo vinavyoaminika, hatua itakayosaidia kudhibiti tatizo la chanjo zisizo halali sokoni.

Bi. Ester Munuo, muuzaji wa pembejeo za mifugo mkoani humo, alisema kuwa pamoja na chanjo ya Newcastle (TEMEVAC), kuna umuhimu wa TVLA kuongeza uzalishaji wa aina nyingine za chanjo za kuku, zikiwemo chanjo za gumboro na ndui, ili kuwapa wauzaji uhakika wa chanzo sahihi cha chanjo.

“Tunapopata chanjo kutoka mamlaka moja inayoaminika, inatusaidia kuepuka kuchukua chanjo kutoka vyanzo visivyo na uhakika, jambo ambalo linaweza kuleta changamoto kwa mtumiaji na kuathiri imani ya wafugaji,” alisema.

Kwa upande wake, Bw. Anthony Ntobi alisema kuwa upatikanaji wa chanjo kwa wakati na kupitia mamlaka rasmi utarahisisha kazi ya wauzaji na kuongeza ufanisi kwa wafugaji.

“Kuna baadhi ya chanjo za kuku ambazo wakati mwingine husambazwa kwa nyakati tofauti. Kupata chanjo moja kwa moja kutoka mamlaka husika kutarahisisha upatikanaji, kupunguza hatari ya chanjo feki na kutuwezesha kuwahudumia wafugaji kwa ufanisi zaidi,” alisema.

TVLA imeeleza kuwa itaendelea kutoa elimu kwa umma na wadau wa sekta ya mifugo katika mikoa mbalimbali nchini kama sehemu ya mkakati endelevu wa kitaifa wa kuimarisha afya za mifugo, kuongeza uzalishaji na kuchangia maendeleo ya sekta ya mifugo nchini.
Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Kanda ya Kati, Dodoma, Dkt. Japhet Nkangaga (kushoto), akitoa elimu kwa muuzaji wa pembejeo za mifugo Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni, Bi. Stella Kahimba, kuhusu taratibu za upatikanaji wa leseni za uuzaji wa viuatilifu vya rejareja na jumla, wakati wa ziara ya uhamasishaji kwa wauzaji wa pembejeo za mifugo iliyofanyika tarehe 20 Februari 2026 mkoani Singida.
Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Kanda ya Kati, Dodoma, Dkt. Japhet Nkangaga (wa pili kutoka kulia), akitoa elimu kwa muuzaji wa pembejeo za mifugo Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni, Bi. Zainabu Ayubu (wa pili kutoka kushoto), kuhusu matumizi sahihi ya chanjo ya Matone (TEMEVAC), ikiwemo namna bora ya kuzipokea, kuzihifadhi na kuzitumia kwa ufanisi, wakati wa ziara ya uhamasishaji iliyofanyika tarehe 20 Februari 2026 mkoani Singida. Wa kwanza kushoto ni Bw. Charles Wambula Afisa Mifugo Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni.
Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Kanda ya Kati, Dodoma, Dkt. Japhet Nkangaga (kulia), akitoa elimu kwa muuzaji wa pembejeo za mifugo Halmashauri ya Wilaya ya Itigi, Bi. Dorcus Sumary, kuhusu matumizi sahihi ya chanjo ya Matone (TEMEVAC) pamoja na taratibu za upatikanaji wa leseni za uuzaji wa viuatilifu vya rejareja na jumla, wakati wa ziara ya uhamasishaji iliyofanyika tarehe 20 Februari 2026 mkoani Singida.
Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Kanda ya Kati, Dodoma, Dkt. Japhet Nkangaga (katikati), akitoa elimu kwa muuzaji wa pembejeo za mifugo Halmashauri ya Wilaya ya Itigi, Bw. Sifael Marko (kushoto), kuhusu matumizi sahihi ya chanjo ya Matone (TEMEVAC) pamoja na taratibu za upatikanaji wa leseni za uuzaji wa viuatilifu vya rejareja na jumla, wakati wa ziara ya uhamasishaji iliyofanyika tarehe 20 Februari 2026 mkoani Singida.

Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Kanda ya Kati, Dodoma, Dkt. Japhet Nkangaga, akitoa elimu kwa muuzaji wa pembejeo za mifugo Manispaa ya Singida, Bw. Abeid Hassan, kuhusu taratibu za upatikanaji wa leseni za uuzaji wa viuatilifu vya rejareja na jumla, wakati wa ziara ya uhamasishaji kwa wauzaji wa pembejeo za mifugo iliyofanyika tarehe 19 Februari 2026 mkoani Singida.
*Ni za wakulima wa kahawa AMCOS ya Mwika Kinyamvuo

*Akagua ujenzi wa hospitali ya Halmashauri ya Manispaa ya Moshi

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amemuagiza Mrajisi wa Vyama vya Ushirika mkoa wa Kilimanjaro ahakikishe Chama cha Ushirika Mkoa wa Kilimanjaro (KNCU) kinalipa kwa mkupuo mmoja sh. milioni 400 ambazo chama hicho kinadaiwa na wakulima.

Ametoa agizo hilo leo (Ijumaa, Februari 20, 2026) aliposimama kusalimia wananchi katika eneo la Chekereni ambapo mkazi wa eneo hilo, Bi. Glory Sam kutoka Chama cha Mwika Kinyamvuo AMCOS alieleza malalamiko yake mbele ya Waziri Mkuu akitaja kusikitishwa na KNCU kuuza kahawa yao msimu wa mwaka 2021/2022 lakini hadi sasa hawajalipwa.

“Tuliuza kahawa yetu kwa zaidi ya shilingi milioni 600 lakini mpaka sasa tumelipwa shilingi milioni 200 pekee. Kwa kipindi chote hicho tumekuwa tukidai milioni 400 bila mafanikio.”

Dkt. Mwigulu amemtaka Mrajis ahakikishe kuwa hadi kufikia tarehe 25 Februari, 2026 Bodi hiyo iwe imekaa kikao na iamue ni mali gani zinauzwa ili kuweza kuwalipa kwa mkupuo wakulima hao.

“Tafuta kimojawapo kiuzwe, shilingi milioni 400 ipatikane na hawa watu walipwe mara moja. Hatuwezi kukaa na jambo moja miaka yote, kama kuna chama hakiwezi kulipa watu mnakaa nacho cha nini? Wananchi wanaumia, tabia ya kuzoea shida, matatizo na machozi ya watu hatuwezi kuivumilia.”

“Jambo limekaa miaka mitano mnataka likae miaka mingapi, upuuzi huu sitaki kusikiliza mnalipa lini? Jumatano ijayo mkae mtoke na majibu, tafuteni mtakachouza muwalipe watu pesa zao,” amesisitiza.

Wakati huohuo, Waziri Mkuu amekagua mradi wa ujenzi wa hospitali ya Halmashauri ya Manispaa ya Moshi inayojengwa katika Kata ya Ng’ambo kwenye manispaa hiyo.

Mradi huo ambao hadi kukamilika kwake unatarajiwa kugharimu sh. bilioni 6.59, hadi sasa ujenzi wake umefikia asilimia 55 ya katika majengo ya huduma za wagonjwa wa nje, huduma za mama na mtoto kwa miundombinu ya sakafu ya chini na ya kwanza.


MKUU wa Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA), Prof. Eliamani Sedoyeka, amesema vijana wengi wanashindwa kufanikiwa katika kujiajiri si kwa kukosa taaluma, bali kwa kukosa maarifa mapana ya uendeshaji wa biashara.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Ijumaa, Februari 20, 2026, Mtumba jijini Dodoma, Prof. Sedoyeka alieleza kuwa pamoja na vijana wengi kuwa na ubunifu na ujuzi katika fani mbalimbali kama teknolojia na utoaji huduma, changamoto huanza wanapokutana na masuala ya fedha na usimamizi.

Alifafanua kuwa ukosefu wa uelewa wa upangaji wa bajeti, usimamizi wa mapato na matumizi, pamoja na mbinu za kuongoza rasilimali watu, umekuwa kikwazo kikubwa kwa ukuaji na uimara wa biashara za vijana.

“Wapo vijana wenye mawazo mazuri na bidhaa zenye ubora, lakini wanaposhindwa kusimamia fedha na mifumo ya kiutawala, biashara zao hushindwa kudumu,” alisisitiza.

Kwa mujibu wake, biashara nyingi huanzishwa kwa ari na matumaini makubwa, lakini hukosa misingi imara ya kiutawala na kifedha inayoweza kuziwezesha kukua na kushindana sokoni.

Akizungumzia suluhisho, Prof. Sedoyeka alisema IAA imeandaa mkakati wa kitaaluma kupitia programu ya “Degree 360”, unaolenga kuwajengea wanafunzi uelewa jumuishi unaohusisha masuala ya fedha, uongozi, usimamizi wa rasilimali watu na mikakati ya biashara.

Alisema lengo la programu hiyo ni kuwaandaa vijana kuwa na uwezo wa kuanzisha na kuendesha miradi au taasisi kwa ufanisi na uendelevu.

Aidha, aliwahimiza vijana kutambua kuwa mafanikio katika kujiajiri yanahitaji zaidi ya kipaji au taaluma pekee; yanahitaji nidhamu ya kifedha, uongozi bora na maarifa sahihi ya biashara.



    
*Asema yatahitajika madarasa 39,000 kukidhi mtaala mpya

*Akagua barabara ya Spencon - Mabogini -Kahe - Chekereni

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amewaagiza watendaji wanaosimamia sekta ya elimu kuanzia sasa waanze kujenga shule zitakazokidhi mahitaji ya mtaala mpya wa elimu ifikapo mwaka 2028.

“Tulikuwa na vikao hivi karibuni, niliagiza ujenzi wa shule za sekondari nchini kuanzia sasa hivi uzingatie kuna madarasa 10 na shule zinapoenda kujengwa pawe na eneo la kutosha kujenga yote 10 au tuamue kujenga madarasa matatu kwenye yale saba yaliyokuwepo,” amesema.

Ametoa agizo hilo leo (Ijumaa, Februari 20, 2026) wakati akizungumza na wananchi wa Mabogini mara baada ya kukagua ujenzi wa barabara ya Spencon - Mabogini - Kahe hadi Chekereni wilayani Moshi, mkoani Kilimanjaro. Alikuwa akijibu ombi la Mbunge wa Moshi Vijijini, Morris Makoi ambaye aliomba kata hiyo ipatiwe sekondari.

Amesema mabadiliko ya mtaala wa elimu yanajumuisha miaka sita ya elimu ya msingi na miaka minne ya elimu ya sekondari. “Zamani tulizoea kusema kila kata iwe na shule ya sekondari lakini tuendako sasa itabidi kila kijiji kiwe na shule ya sekondari ili kumudu mahitaji hayo mapya.”

“Kama tuna bajeti ya kujenga majengo ya elimu, tuanze kuzingatia mitaala mipya. Kati ya mwaka 2026 na 2027, tunapaswa kuongeza madarasa 39,000 kwa maana kwamba tuna vijiji 13,000 na kila shule moja ya msingi itabidi iongezwe madarasa matatu.”

"Tunaposema kuanzia mwaka kesho, mwaka kesho wa bajeti hauko mbali. Ni miezi minne ijayo sababu mwaka mpya wa fedha unaanza Julai, mwaka huu. Na mwaka kesho, darasa la sita na la saba wataunganishwa na kufanya mtihani mmoja ili kujiandaa kuanza elimu ya lazima,” amesema.

Mapema, akielezea hoja kuhusu ujenzi wa barabara hiyo yenye urefu wa kilomita 31.25, Dkt. Mwigulu aliwaelekeza viongozi wa mkoa na wilaya wafuate utaratibu wa kuomba barabara hiyo ipandishwe hadi kutoka TARURA na kwenda TANROADS ili ijengwe kwa kiwango cha lami.

RC na DC, TARURA na TANROADS fanyeni mchakato wa kuipandisha hadhi ya TANROADS ili ijengwe kw amara moja. Kwa muundo wake, barabara hii ni Bypass, kwa hiyo itasaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza msongamano katikati ya mji wa Moshi na pia itasaidia kutoa huku mazao ya wakulima.”

Barabara ya Spencon - Mabogini - Kahe hadi Chekereni inapita katikati ya vijiji 12 ambavyo ni Mabogini, Chekereni, Mtakuja, Oria, Miwaleni, Kahe, Mwangaria, Ngasini, Ngasini B, Soko, Kyomu na Gona.

Kwa mujibu wa taarifa ya ujenzi iliyosomwa mbele ya Waziri Mkuu, barabara hiyo ambayo itagharimu sh. bilioni 7.2, iko chini ya mtandao wa barabara wa TARURA Wilaya ya Moshi na inapita katika majimbo matatu ya Moshi Manispaa, Moshi Vijijini na Vunjo. Aidha, inapita katika kata tatu za Kahe Magharibi, Kahe Mashariki na Mabogini.

Ujenzi wa barabara hiyo utasaidia kuimarisha shughuli za usafiri na usafirishaji na kuchochea uchumi kwenye maeneo yaliyo pembezoni mwa barabara hii kutokana na uwepo wa maeneo ya kilimo cha mpunga na mbogamboga.

Naibu Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile, amesema maendeleo ya mradi wa ukarabati wa Meli ya MV Liemba mkoani Kigoma yanaridhisha na utekelezaji wake umefikia zaidi ya asilimia 55. 

Kihenzile amesema hayo leo katika ziara ya kukagua miradi ya maendeleo mkoani Kigoma ambapo Naibu waziri huyo ameeleza kuridhishwa na kasi ya ukarabati huo na kusisitiza umuhimu wa meli hiyo katika kuchochea uchumi na kurahisisha usafiri katika Ziwa Tanganyika.

 Aidha, Kihenzile amepata fursa ya kutembelea boti ya utafutaji na uokoaji iliyonunuliwa na Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania. Alifafanua kuwa boti hiyo itasaidia kuongeza uwezo wa kukabiliana na ajali za majini, matukio ya dharura pamoja na vitendo vya uhalifu katika Ziwa Tanganyika.

Pia Naibu waziri huyo ameeleza kuwa uwekezaji huo una lengo la kuimarisha usalama wa wasafiri na mali zao, sambamba na kuboresha huduma za usafiri majini, huku akisisiitiza kuwa serikali itaendelea kuwekeza katika miundombinu ya usafiri ili kuhakikisha sekta hiyo inachangia kikamilifu maendeleo ya taifa.

Katika hatua nyingine, Kihenzile ametembelea mradi wa ujenzi wa kiwanja cha ndege mkoani humo, ambapo utekelezaji wake unaendelea vizuri na kuridhishwa na hatua zilizofikiwa katika miradi yote aliyokagua na kuwataka wasimamizi kuhakikisha inakamilika kwa wakati na kwa viwango vinavyotakiwa.














Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amefika katika makazi ya Kiaskofu ya Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, Kurasini, kuwasilisha salamu za rambirambi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kufuatia kifo cha Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo.

Makamu wa Rais akizungumza na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, Mhashamu Askofu Yude Thaddeus Ruwa’ich (OFM Cap), amesema Rais Samia ameguswa na msiba huo na kuahidi kushirikiana bega kwa bega na Kanisa Katoliki katika msiba huo.

Amesema Serikali inatambua mchango mkubwa aliyoutoa Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo katika kipindi cha miaka 42 ya utumishi wake na nia ya Serikali ni kuona kwamba Kardinali Pengo anazikwa kwa heshima zote.

 Kwa upande wake Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, Mhashamu Askofu Yude Thaddeus Ruwa’ich (OFM Cap), ameishukuru Serikali kwa mchango iliyotoa wakati wa matibabu ya Kardinali Pengo.

Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, alifariki tarehe 19 Februari 2026 katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) Jijini Dar es Salaam. 







Na WAF-Morogoro

Serikali kupitia Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa lisilo la kiserikali linalojikita katika kuongeza upatikanaji wa elimu kwa wasichana na kuwainua vijana wa kike kupitia elimu, uongozi na uwezeshaji wa kiuchumi (CAMFED) kwa mafunzo elekezi kuhusu miradi inayoisadia kufanikisha malengo na mipango yake kwa.ngazi ya msingi na taifa kwa ujumla.

Akizungumza wakati wa kutoa mafunzo hayo Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la CAMFED Bi. Anna Sawaki amesema kuwa Serikali kupitia Wizara ya Afya imekuwa kiungo muhimu cha utekelezaji wa miradi ya afya na Shirika kwa kuendelea kuboresha mazingira ya afya mashuleni na kufungua fursa za ajira za sekta ya afya.

"Kupitia fursa za ajira zinazotangazwa na Serikali, Wizara ya Afya, jumla ya Wafadhiliwa 141 wa CAMFED wameajiriwa katika kada za ukunga na uuguzi," amesema Bi. Sawaki.

Ameongeza kuwa Wizara ya Afya na wafadhiliwa wanashiriki kwenye miradi kama vile School Water Sanitation and Hygiene (SWASH) inayolenga kutoa mafunzo ya usafi binafsi mashuleni, kuweka mbinu rafiki za kujikinga na mazingira hatarishi ikiwemo kupata ujauzito katika umri mdogo.

Aidha, amesema kuwa CAMFED itaendelea kushirikiana na Serikali kupitia Wizara ya Afya ambapo ushirikiano huo unatekelezwa chini ya Hati ya Makubaliano (MoU) kati ya pande hizo mbili, inayolenga kuunganisha juhudi za sekta ya afya na elimu ili kuhakikisha jamii inanufaika na huduma bora na endelevu za afya.

Wizara ya Afya na CAMFED zitaendeleza ushirikiano wao ambao ni ishara ya dhamira ya pamoja ya kuhakikisha huduma za afya ngazi ya msingi zinaimarika, huku jamii ikiwezeshwa kupitia elimu na maendeleo endelevu, ambapo malengo ya sasa ni kuanzisha huduma za ufadhili katika Halmshauri zipatazo 41 na kuunda jumla ya Halmashauri 76 zitakazotekeleza miradi hiyo.

Mafunzo hayo yametolewa Februari 19, 2026 Mkoani Morogoro, kwa Maafisa Habari wa Wizara ya Afya, Kilimo, Elimu Sayansi na Teknolojia, TAMISEMI, Vijana na Ajira, Maendeleo ya Jamii, na Maafisa Habari wa Halmashauri za Wilaya 35 za Mikoa 10 zinazotekeleza miradi hiyo.










Top News