WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, ameweka jiwe la msingi la mradi wa ujenzi wa barabara ya Kagwira – Karema (kilometa 112) katika Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika mkoani Katavi.

Mradi huo unatekelezwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) kwa gharama ya takribani shilingi bilioni 219.09, ukiwa na lengo la kuboresha miundombinu ya usafiri na kuchochea shughuli za kiuchumi katika ukanda wa Ziwa Tanganyika.

Kwa mujibu wa taarifa ya mradi iliyosomwa na Kaimu Meneja wa Udhibiti wa Miradi TANROADS, Mhandisi Malima Musema Mongo, ujenzi wa barabara hiyo umegawanyika katika vipande viwili ambavyo ni Kagwira – Kasekese (kilometa 54.144) na Kasekese – Ikola – Karema (kilometa 56.911).

Alisema ujenzi wa kipande cha Kagwira – Kasekese unagharimu takribani shilingi bilioni 106.95 na umefikia asilimia 8.2 ya utekelezaji, huku kipande cha Kasekese – Ikola – Karema kikigharimu takribani shilingi bilioni 112.14 na kufikia asilimia 33.4 ya utekelezaji.

Mradi huo ni wa kimkakati kwa kuwa utarahisisha usafirishaji wa mizigo kupitia Bandari ya Karema kwenda nchi jirani ikiwemo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, pamoja na kupunguza msongamano wa malori ya mizigo katika eneo la Tunduma.

Aidha, barabara hiyo itarahisisha usafirishaji wa mazao kutoka mashambani na kuwaunganisha wananchi na huduma mbalimbali za kijamii kama vile huduma za afya na biashara katika maeneo ya ukanda huo.

Mradi huo unatekelezwa kwa mfumo wa kimkataba na unatarajiwa kukamilika ndani ya kipindi cha miezi 26. Hadi sasa utekelezaji wa jumla wa mradi umefikia asilimia 21, ambapo kiasi cha shilingi bilioni 32.37 kimeshapokelewa na kutumika katika hatua mbalimbali za ujenzi.

Kukamilika kwa mradi wa barabara ya Kagwira – Karema kunatarajiwa kuwa kichocheo muhimu cha maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika Mkoa wa Katavi na maeneo jirani kwa kuimarisha usafiri, biashara na mawasiliano katika ukanda wa Ziwa Tanganyika.








Kamati ya kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii imempongeza Afisa Uhifadhi Mkuu wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro Dkt. Agnes Gidna kutokana na umahiri, umakini, kujiamini na uchambuzi wake mkubwa wa masuala ya mambo kale na jiolojia.

Wakiongozwa na mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Timotheo Mnzava wabunge hao wametoa pongezi hizo baada ya kukagua na kupata maelezo ya mradi wa makumbusho ya Urithi Geopark Museum. 

Wabunge wamepongeza kazi kubwa iliyofanywa na serikali ya Tanzania na China ambapo hawakusita kuelezea hisia zao kutokana na mtaalam huyo  alivyowakonga nyoyo kwa kuelezea historia kuhusa kutokea kwa kreta ya Ngorongoro, milpuko ya volkano, maumbile ya dunia, chanzo cha binadamu wa kale na masuala mengine.

Kamati ya Bunge imeielekeza wizara ya Maliasili na Utalii kuitumia makumbusho hiyo kama bidhaa ya utalii na kitovu cha elimu kwa vijana wa kitanzania na kimataifa.

Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt.Ashatu Kijaji aliwashukuru wabunge kwa pongezi hizo na kuwahakikishia kuwa wizara yake itasimamia kwa karibu maendeleo ya Urithi Geopark Museum.

Dkt.Agnes Gidna, mtaalam wa makumbusho, mambo kale na urithi wa utamaduni amekuwa kiungo muhimu  katika makumbusho hayo kutokana na umahiri wake wa kitaaluma na kitaalam kuihadithia yaliyopo kwenye makumbusho hiyo.







Na Mwandishi Wetu, Mbeya

MKUU wa Wilaya ya Mbeya, Solomon Itunda, amewahimiza viongozi wa dini ya Kiislamu kuendelea kusimamia na kuimarisha maadili kwa waumini hata baada ya kumalizika kwa mwezi mtukufu wa Ramadhan.

Itunda ametoa wito huo wakati wa hafla ya Iftari iliyoandaliwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, Erica Yegella, iliyolenga kuimarisha mshikamano miongoni mwa waumini, watumishi wa umma na wadau wa maendeleo.

Akizungumza katika hafla hiyo, Itunda amesema maadili yanayojengwa wakati wa Ramadhan yanapaswa kudumishwa katika maisha ya kila siku ili kulinda amani na utulivu wa nchi.

“Niwaombe viongozi wa dini kuendelea kuhamasisha waumini kutenda mema hata baada ya Ramadhan kupita. Kama viongozi wa umma, tunalo jukumu la kuendeleza uadilifu na kuwahudumia wananchi kwa haki,” amesema Itunda.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa amani akieleza kuwa ndiyo nguzo inayowezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo, ukiwemo upanuzi wa barabara kutoka Igawilo hadi Tunduma unaolenga kuimarisha miundombinu ya usafirishaji na biashara.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Erica Yegella, amesema hafla hiyo imekuwa sehemu ya utamaduni wa Halmashauri hiyo kuwakutanisha wadau mbalimbali wakiwemo viongozi wa dini na wafanyabiashara ili kuimarisha ushirikiano katika kuleta maendeleo ya wilaya.

Hii ni mara ya pili kwa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya kuandaa Iftari kwa ajili ya watumishi na wananchi, hatua inayotajwa kusaidia kupunguza mwanya kati ya watendaji wa serikali na jamii wanayoihudumia.








Jumla ya miti 1,500 ya matunda na kivuli imepandwa leo katika Shule ya Msingi Msinjahili, Manispaa ya Lindi, ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha utunzaji wa mazingira na kujiandaa na maadhimisho ya Siku ya Misitu Duniani pamoja na Wiki ya Upandaji Miti Kitaifa itakayofanyika mkoani Lindi.

Zoezi hilo limeongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Lindi, Victoria Mwanziva, ambaye amewahimiza wananchi, wanafunzi na taasisi mbalimbali kuendelea kushiriki kikamilifu katika kampeni ya upandaji miti ili kulinda mazingira na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Mwanziva amesema kuwa miti ina mchango mkubwa katika kuhifadhi mazingira, kuboresha hali ya hewa na kutoa manufaa mbalimbali ikiwemo matunda, kivuli na malighafi muhimu kwa jamii. Amesisitiza kuwa kila mwananchi ana wajibu wa kupanda na kuitunza miti ili kuhakikisha mazingira yanabaki salama kwa kizazi cha sasa na kijacho.

Akieleza kuhusu kampeni ya upandaji miti pamoja na maandalizi ya maadhimisho ya upandaji miti kitaifa, Saimoni Kipeleja kutoka Idara ya Misitu na Nyuki ya Wizara ya Maliasili na Utalii amesema serikali inaendelea kuhamasisha upandaji miti nchini kama sehemu ya mkakati wa kuongeza uoto wa asili na kukabiliana na uharibifu wa mazingira.

Kipeleja amesema kuwa maadhimisho hayo yanatarajiwa kuwakutanisha wadau mbalimbali wakiwemo viongozi wa serikali, taasisi, wanafunzi na wananchi kwa lengo la kuhamasisha upandaji miti na kuimarisha juhudi za uhifadhi wa misitu.

Awali, Mhifadhi wa Wilaya ya Lindi kutoka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Gaspar Vicent, amesema taasisi hiyo imekuwa ikizalisha miche ya miti zaidi ya laki mbili kila mwaka na kuigawa kwa taasisi mbalimbali pamoja na watu binafsi ili kuongeza kasi ya upandaji miti katika jamii.

Vicent amebainisha kuwa ushirikiano wa wananchi ni muhimu katika kuhakikisha miti inayopandwa inatunzwa ipasavyo ili kufikia malengo ya kuongeza uoto wa asili na kulinda rasilimali za misitu. Zoezi hilo la upandaji miti limehudhuriwa na viongozi wa serikali, walimu, wanafunzi pamoja na wadau wa mazingira. 

Maadhimisho ya Siku ya Misitu Duniani na Kampeni ya upandaji miti Kitaifa yanaenda sambamba na Kauli mbiu isemayo Misitu ni uchumi endelevu,Tuhifadhi kwa Maendeleo ya Taifa.









 


Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi Asilia, Dkt. James Mataragio, ameitaka Menejimenti ya Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kuhakikisha kuwa miradi ya mafuta na gesi asilia inayoendelea nchini inatekelezwa na kukamilika kwa wakati ili iweze kuendelea kuchangia kikamilifu katika maendeleo ya uchumi wa taifa.


Dkt. Mataragio ametoa maelekezo hayo leo wakati alipokutana na menejimenti ya TPDC  kwa lengo la kujadili fursa zilizopo katika sekta ya Mafuta  na Gesi Asilia, changamoto pamoja na kuweka mikakati madhubuti ya kuimarisha sekta.

Aidha, Dkt. Mataragio ameiagiza TPDC, kuongeza vitalu vipya vya uwekezaji ili kuvutia wawekezaji zaidi katika shughuli za utafutaji na uzalishaji wa mafuta na gesi asilia.

“Ni muhimu TPDC ikaendelea kupanua maeneo ya uwekezaji ili kuvutia wawekezaji zaidi katika shughuli za utafutaji na uzalishaji wa mafuta na gesi asilia kama mnavyofahamu rasilimali hii ni muhimu katika kutoa uhakika wa nishati nchini mfano kwenye  uzalishaji wa umeme na kukuza uchumi wa viwanda." Amesisitiza Dkt.Mataragio

Kwa upande wake, Kamishna wa Petroli, Goodluck Shirima, amesema Serikali inaendelea kuimarisha miundombinu ya usambazaji wa gesi asilia ili kuongeza matumizi yake katika sekta mbalimbali ikiwemo majumbani, viwandani na katika uzalishaji wa umeme.

Ameongeza kuwa Serikali inaendelea kutenga na kuandaa maeneo kwa ajili ya ushiriki wa sekta binafsi kwenye miradi ya usambazaji wa gesi, akibainisha kuwa miradi hiyo ni miongoni mwa miradi mikubwa ya kimkakati (flagship projects) inayolenga kuongeza matumizi ya gesi asilia.

Naye,  Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Mussa Makame amesema Shirika hilo litaendelea kutekeleza maagizo  yanayotolewa na viongozi wa Wizara kwa lengo la kuzidi kuiimarisha sekta ya Mafuta na Gesi Asilia.

“TPDC itaendelea kufanya kazi kwa karibu na Wizara ya Nishati ili kuhakikisha miradi ya gesi asilia na mafuta inatekelezwa kwa ufanisi na kwa manufaa ya Watanzania wote."  Amesema Makame

Ziara ya Dkt. Mataragio TPDC ni muendelezo wa ziara zake katika Taasisi zinazosimamia Sekta ya Mafuta na Gesi Asilia ikiwa ni sehemu ya jitihada za Wizara ya Nishati kuimarisha usimamizi wa taasisi zake ili ziendelee kutekeleza majukumu kwa ufanisi lengo likiwa ni kuhakikisha wananchi wananufaika  na rasilimali zilizopo nchini.







Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amekutana na Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa, Mhe.Ali Mwadini, kujadili mikakati ya kuvutia na kutafuta wawekezaji katika eneo la Bonde  la Msimbazi lililopo jijini Dar es Salaam.

Katika mazungumzo hayo, viongozi hao wamekubaliana kuwa na mpango madhubuti wa kutafuta wawekezaji wa kimataifa watakaoshiriki kuwekeza katika maendeleo ya bonde hilo, ambalo Serikali imeanza kulijenga ili kupunguza athari za mafuriko na wakati huo huo kufungua fursa mpya za uwekezaji na biashara.

Utekelezaji wa mpango huo unatarajiwa kuchochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi, kuboresha huduma za kijamii pamoja na kuongeza fursa za ajira kwa wananchi wa jiji la Dar es Salaam na maeneo jirani, huku pia ukivutia wafanyabiashara na wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi.

Prof. Shemdoe amefanya ziara katika ofisi za Ubalozi wa Tanzania nchini Ufaransa jana Machi 13, 2026, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono jitihada za Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuhakikisha uwekezaji unaofanyika katika Bonde la Msimbazi unaleta manufaa makubwa kwa uchumi wa taifa na kuwawezesha wajasiriamali na wafanyabiashara wa jijini Dar es Salaam.

Uwekezaji unaotarajiwa katika bonde hilo ni sehemu ya mikakati ya Serikali ya kuendeleza miundombinu ya kisasa mijini, kudhibiti mafuriko na kuifanya Dar es Salaam kuwa kitovu muhimu cha biashara na uwekezaji katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Na Mwandishi Wetu

Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, amewahimiza wananchi wa wilaya hiyo kuendelea kudumisha umoja, mshikamano na utamaduni wa kusaidiana katika jamii, hususan katika kipindi hiki cha kuelekea sikukuu ya Eid al-Fitr.

Wito huo ameutoa wakati wa hafla maalumu ya Iftar iliyoandaliwa na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Handeni, hafla iliyokwenda sambamba na harambee ya kuchangia makundi maalumu yenye uhitaji ambapo Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Balozi Dkt. Batilda Burian amechangia Sh. milioni moja.

Akizungumza katika hafla hiyo, iliyowakutanisha viongozi wa serikali, viongozi wa dini na wananchi, Mhe. Nyamwese amesema kuwa Iftar hiyo imelenga kuimarisha uhusiano mzuri kati ya viongozi na wananchi pamoja na kukuza utamaduni wa kusaidiana na kushirikiana katika jamii.

Amesema mshikamano na umoja wa wananchi ni msingi muhimu katika kudumisha amani, utulivu na maendeleo ya wilaya ya Handeni, hivyo ni muhimu kila mmoja kuchukua nafasi yake katika kusaidia wenye uhitaji.

Aidha, amewataka wananchi kuendelea kuwa na moyo wa huruma na kusaidia makundi maalumu kama yatima, wazee na watu wenye mahitaji maalumu, akisisitiza kuwa hatua hiyo ina mchango mkubwa katika kuimarisha ustawi wa jamii.

Awali, kabla ya hafla hiyo Mhe. Nyamwese ametembelea Gereza la Wilaya ya Handeni na kutoa msaada wa vitu mbalimbali kwa wafungwa ikiwa ni kuwaonesha upendo kwao katika kipindi hiki cha kuelekea sikukuu ya Eid al-Fitr.


Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) imeandaa futari maalum kwa watoto wenye uhitaji kutoka Kituo cha Kulea Watoto wenye Uhitaji cha Zili, tukio lililolenga kuimarisha mshikamano wa kijamii na kuendeleza ujumuishi kwa makundi yenye mahitaji maalum.

Hafla hiyo ilifanyika katika Makao Makuu ya TCAA jijini Dar es Salaam, na kuhudhuriwa na wadau wa sekta ya usafiri wa anga, watumishi wa TCAA pamoja na watoto wenye uhitaji. Wageni walishiriki futari kwa pamoja na watoto hao, pamoja na kukabidhi zawadi kama ishara ya upendo, mshikamano na uwajibikaji wa kijamii.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mgeni Rasmi Naibu Waziri wa Uchukuzi Mhe. David Kihenzile, aliyemwakilisha Waziri wa Uchukuzi, alipongeza jitihada za TCAA katika kuchangia maendeleo ya jamii akisisitiza umuhimu wa taasisi za umma kushiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii, hususan zinazolenga kuwajali watoto wenye uhitaji.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TCAA, Salim Msangi alisisitiza kuwa pamoja na jukumu la kusimamia na kudhibiti sekta ya usafiri wa anga, mamlaka itaendelea kutekeleza miradi ya kijamii inayolenga kugusa maisha ya wananchi na kukuza maadili ya utu, mshikamano na usawa.

Kupitia futari hii maalum, TCAA imeendelea kudhihirisha kuwa sekta ya usafiri wa anga siyo tu kuhusu usimamizi na kanuni, bali pia ni chombo muhimu cha kujenga jamii jumuishi, yenye huruma na mshikamano.
Naibu Waziri wa Uchukuzi David Kihenzile pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) Salim Msangi wakikabidhi mkono wa mwezi mtukufu kwa  watoto wenye uhitaji kutoka Kituo cha Kulea Watoto wenye Uhitaji cha Zili ikiwa ni kuimarisha mshikamano wa kijamii na kuendeleza ujumuishi kwa makundi yenye mahitaji maalum.
Naibu Waziri wa Uchukuzi David Kihenzile  akitoa neno wakati wa futari iliyoandaliwa na Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA)
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) Salim Msangi akizungumza na baadhi ya wafanyakazi wa TCAA, wadau mbalimbali wa Usafiri wa Anga pamoja na watoto wenye uhitaji kutoka Kituo cha Kulea Watoto wenye Uhitaji cha Zili wakati wa hafla ya futari iliyoandaliwa na TCAA.
Baadhi ya wafanyakazi wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), wadau mbalimbali wa Usafiri wa Anga pamoja na watoto wenye uhitaji kutoka Kituo cha Kulea Watoto wenye Uhitaji cha Zili wakiwa kwenye hafla ya futari iliyoandaliwa na TCAA.
Mjumbe wa Bodi ya TCAA Vuai A. Hilal akitoa neno la shukrani  kwenye hafla ya futari iliyoandaliwa na TCAA.
Picha za pamoja

Top News