-Wachimbaji, Wakandarasi Kunufaika na Mpango Mpya wa NMB na Mantrac

DAR ES SALAAM. Benki ya NMB na Mantrac Tanzania Limited zimesaini Hati ya Makubaliano ya Ushirikiano itakayorahisisha upatikanaji wa mikopo ya kununua na kuhudumia mitambo kwa wachimbaji, wakandarasi na wafanyabiashara katika sekta za madini, ujenzi, miundombinu, nishati na viwanda.

Makubaliano hayo yalisainiwa jijini Dar es Salaam na Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB, Filbert Mponzi, pamoja na Mkurugenzi wa Biashara na Uendeshaji wa Mantrac Kanda ya Afrika Mashariki, Levite Dongmo. Ushirikiano huo unaunganisha uwezo wa kifedha wa NMB, yenye matawi zaidi ya 250 nchini, na utaalamu wa Mantrac katika mitambo na huduma za kiufundi.

Mponzi alisema wateja watakaokidhi vigezo wataweza kupata ufadhili kwa kutoa mchango wa awali wa kati ya asilimia 20 na 25, huku ratiba za marejesho zikiandaliwa kulingana na mtiririko wa fedha na mazingira ya biashara. Mitambo itakayofadhiliwa itakuwa na dhamana ya kati ya miezi 24 na 36 kulingana na masharti yatakayoidhinishwa.

Dongmo alisema ushirikiano huo utaongeza upatikanaji wa mitambo, majenereta, matengenezo na huduma baada ya mauzo. Mpango huo unatarajiwa kuongeza uzalishaji, kupunguza kusimama kwa miradi na kuelekeza mitaji zaidi katika sekta zinazozalisha ajira na kuchochea ukuaji wa uchumi.
Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB, Filbert Mponzi (kulia), na Mkurugenzi wa Biashara na Uendeshaji wa Mantrac Kanda ya Afrika Mashariki, Levite Dongmo, wakisaini Hati ya Makubaliano ya Ushirikiano itakayorahisisha ufadhili wa mitambo kwa wachimbaji, wakandarasi na wafanyabiashara katika sekta za madini, ujenzi na miundombinu, jijini Dar es Salaam.

Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB, Filbert Mponzi (kulia), na Mkurugenzi wa Biashara na Uendeshaji wa Mantrac Kanda ya Afrika Mashariki, Levite Dongmo, wakipeana mkono baada ya kubadilishana Hati ya Makubaliano ya Ushirikiano wa ufadhili wa mitambo, jijini Dar es Salaam.

Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa uhifadhi anayesimamia huduma za Utalii na Masoko, Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro Mariam Chuma Kobelo, ametunukiwa tuzo ya Iconic Woman in Tourism Promotion katika hafla ya Ladies Talk Awards & Dinner 2026 iliyofanyika usiku wa kuamkia leo mjini Morogoro.

Bi Mariam ametwaa tuzo hiyo kwa kutambua mchango wake mkubwa katika kuendeleza na kutangaza utalii wa Tanzania kupitia ubunifu wa kampeni za masoko, usimamizi wa huduma za utalii, pamoja na juhudi za kukuza utalii wa ndani na wa kimataifa kupitia eneo la Hifadhi ya Ngorongoro.

Kupitia uongozi wake, Ngorongoro imeendelea kujijengea sifa kama moja ya vivutio vya utalii wa kifahari (Premium destination) vinavyoongoza barani Afrika, na kusimamia utekelezaji wa kampeni mbalimbali za masoko zinazolenga kuongeza idadi ya watalii na kuhamasisha ushiriki wa jamii katika maendeleo ya utalii endelevu.

Utambuzi huo unaongeza rekodi ya mafanikio ya kamishna Kobelo, ambaye amekuwa mstari wa mbele katika kutafuta masoko mapya ya utalii wa Ngorongoro ndani na nje ya nchi, pamoja na kuratibu programu zinazochangia ukuaji wa sekta ya utalii na kuimarisha juhudi za uhifadhi.

Kamishna Mariam Kobelo ameishukuru Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro chini ya usimamizi wa kamishna wa uhifadhi wa mamlaka hiyo Abdul-Razaq Badru kutokana na ushirikiano mkubwa katika kukuza vipaji vya watumishi na kuviendeleza.






Mkuu wa Wilaya ya Mufindi mheshimiwa Dkt. Linda Salekwa akiwa ameongozana na viongozi wa Mufindi ametembelea na kukagua maonesho ya 88 Mkoa wa Iringa katika Eneo la Kihesa Kilolo Iringa.

Amesema  wajasiriamali wengi wana bidhaa bora ambazo zinatakiwa kutangazwa kwa nguvu ili bidhaa hizo zipate masoko nje ya Nchi na Mikoa mbalimbali . 

Aidha amekagua teknolojia mbalimbali ambazo zipo kwaajili ya kurahisisha ubareshaji wa utendaji wa kazi wa mkulima au mfugaji katika maonesho hilo na kushauri ziuzwe kwa gharama nafuu ili wakulima na wafugaji waweze kumudu na kuboresha shughuli zao.

Aidha katika maonesho hayo Dc-Mufindi amepata fursa ya kutembelea banda la Halmashauri ya Mji Mafinga na kuweza kuzungumza na wakulima na wafugaji akiwa ameongozana na Mkurugenzi wa Mji Mafinga Bi Fidelica Myovella na Mwenyekiti wa Mji Mafinga, Mheshimiwa Regnant Kivinge.








Wakati wakongwe wa Redio Tanzania wakiadhimisha miaka 75 ya utangazaji Tanzania Bara na miaka 61 ya Redio Tanzania wamewataka waandishi na watangazaji vijana kuendelea kulinda misingi ya uandishi bora kwa kuzingatia maadili, utafiti, Kiswahili sanifu na matumizi sahihi ya teknolojia.

Katika kongamano la kuwakutanisha wakongwe wa Radio Tanzania (RTD), lililofanyika Dar es Salaam leo Julai 18,2026 wadau mbalimbali wa habari wameeleza kuwa pamoja na mabadiliko makubwa yaliyotokana na maendeleo ya teknolojia, msingi wa taaluma ya habari bado unabaki kuwa ukweli, weledi na uwajibikaji kwa jamii.

Mwenyekiti wa wakongwe wa RTD Suleiman Kumchaya amesema vijana wanaochipukia wamekuwa hawana matumizi sahihi ya lugha ya Kiswahili wanapokuwa wakiwasilisha kazi za kihabari na kuwahimiza kuwa pamoja na maendeleo ya teknolojia, bado kuna umuhimu wa kulinda ubora wa lugha ya Kiswahili katika uandishi na utangazaji.

Amesema: " Tunaona na kusikia sasa hivi watangazaji wanakibananga sana kiswahili. Tumeweka msingi wa kuendelea kushirikiana na vijana ili kuhakikisha maadili, weledi na ubora wa kazi vinaendelea kuwa nguzo ya tasnia ya habari,"

Mkongwe wa utangazaji Rose Mwalimu, amesema tofauti kubwa kati ya utangazaji wa zamani na wa sasa ipo katika kiwango cha utafiti, ubunifu na maandalizi ya maudhui.

Amesema enzi zao waandishi walitumia muda mwingi kutafuta taarifa, kufanya utafiti, kuandika script na kutengeneza vipindi vyenye kugusa maisha ya watu, tofauti na baadhi ya maudhui ya sasa ambayo hayana uzito kutokana na kukosa utafiti wa kutosha.

Alisisitiza kuwa utangazaji bora unahitaji ubunifu, hasa kwenye redio ambayo inahitaji mtangazaji kutumia lugha na sauti kujenga picha kwa msikilizaji.

Kwa upande wake, Mary Kafyome, mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), amesema wakongwe wa RTD wameacha alama kubwa katika maendeleo ya taifa kwa kutumia vipawa vyao na weledi katika kipindi ambacho teknolojia haikuwa imeendelea kama ilivyo sasa.

Amesema vijana wanapaswa kujifunza kutoka kwa wakongwe hao kwa kuzingatia kujituma, kuipenda kazi, kuwa waadilifu na kutumia teknolojia kama nyenzo ya kuboresha kazi zao.

“Teknolojia inapaswa kutusaidia kufanya kazi vizuri zaidi, lakini tusiruhusu ichukue nafasi ya ubunifu na misingi ya taaluma,” amesema.

Kwa upande wake, Meneja wa Huduma za Utangazaji wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Kadaya Baluhye, amesema teknolojia imebadili namna habari zinavyotengenezwa na kusambazwa, lakini haiwezi kuchukua nafasi ya maadili ya mwandishi wa habari.

Amesema waandishi wanapaswa kutumia teknolojia kwa ubunifu ili kuelimisha, kuburudisha na kuhabarisha jamii kuhusu masuala muhimu ikiwemo afya, maendeleo ya serikali na maandalizi ya Tanzania kuwa mwenyeji wa mashindano ya AFCON 2027.

Naye mtangazaji wa Bongo FM Radio, Emmy Jovin, amesema jambo kubwa alilojifunza kutoka kwa wakongwe ni umuhimu wa maadili na uzalendo katika utoaji wa taarifa.

Amesema kasi ya mitandao ya kijamii na teknolojia imekuwa ikiwafanya baadhi ya wanahabari kukimbilia kupata watazamaji wengi bila kuzingatia misingi ya taaluma.

Aliongeza kuwa matumizi ya Akili Mnemba (AI) yanapaswa kufanyika kwa umakini huku mwandishi akibaki na jukumu la kuhakiki taarifa na kuhakikisha maudhui yanayowasilishwa yana ukweli na yanazingatia maadili.









Na Mwandishi Wetu.

KATIBU wa Chama cha Mapinduzi (CCM)Wilaya ya Kilosa,Mkoani Morogoro, Janus Mfaume, anatuhumiwa kumdhalilisha na kumtishia maisha mwanachama wa Chama hicho Egon Haule, baada ya kumfukuza ofisini bila sababu za msingi huku akimtolea kauli za vitisho.

Tukio hilo limetokea Julai 17 mwaka huu katika ofisi za Wilaya za Chama hicho ambapo Haule alikwenda kuitikia wito wa Katibu wa Jumuiya ya Wazazi aliyemwita kwa ajili ya kumpa majukumu.

Akizungumza kwa masikitiko makubwa Haule,alisema,hii ni mara ya tatu anafanyiwa udhalilishaji na kutishiwa maisha na Mfaume huku akitishia kumfanyia kitu kibaya ambacho hata kisahau katika maisha yake.

Haule alisema,hana ugomvi wowote na Katibu wake huyo lakini anashangazwa kuona kila siku amekua akimtishia maisha sambamba na kumfukuza kufika katika ofisi za Chama hicho Wilaya.

"Mimi ni mwanachama halali ambaye nimekua nikijitolea majukumu mbalimbali ya Chama kwa mwamvuli wa UVCCM Wilaya lakini napitia manyanyaso na udhalilishaji kwa kufukuzwa kila ninapofika ofsini na nimejaribu mara kadhaa kumuomba Katibu Mfaume anieleze kuna tatizo gani kauli zake amekua akisema hataki kuniona nikifika pale,"

"Kabla ya tukio la juzi nilishamuandikia ujumbe mfupi wa maandishi kumuomba tuonane anieleze nina tatizo gani la kuzuiwa kufika ofsini lakini hajawahi kunijibu,"alisema Haule.

"Kwa masikitiko makubwa huku moyo wangu ukiwa umeelemewa na huzuni na shinikizo kubwa la kukata tamaa katika kuendelea kujifunza uongozi, Itikadi na misingi ya Chama Cha Mapinduzi Ili baadae nami niwe kiongozi sahihi wa UVCCM na hatimaye chama Cha Mapinduzi,'

"Nawasilisha kwenu kitendo cha aibu na udhalilishaji na vitisho alivyo nitendea Ndugu Janus Mfaume Katibu wa CCM Wilaya ya Kilosa Julai 17 mwaka huu nilipofika ofisi ya CCM Wilaya kwa lengo la kumsaidia kazi Katibu wa Jumuiya ya Wazazi Wilaya ambaye alinihitaji nifike hapo," aliandika Haule kupitia kundi sogozi la Chama hicho.

"Nimeamua kuwashirikisha kuhusu changamoto ninayopitia. Katibu wa CCM Wilaya amenieleza nisiende ofisini, na katika mawasiliano yetu kuna kauli nilizozielewa kama vitisho. Nina rekodi ya sauti ya mawasiliano hayo, ambayo niko tayari kuiwasilisha kwa mamlaka husika endapo itahitajika.

Lengo langu si kumhukumu mtu yeyote kupitia kundi hili, bali kuomba suala hili lipatiwe ufumbuzi kwa kuzingatia haki, taratibu za Chama, na misingi ya uongozi wenye uwajibikaji.

"Naomba viongozi mlipokee jambo hili na kulifanyia kazi kwa busara na haki alieleza Haule"

Alipotafutwa Katibu wa CCM Wilaya ya Kilosa, Mfaume kuhusiana na tuhuma hizo alikiri kumfukuza Haule akifafanua kuwa ni kijana ambaye ana mienendo ya kihalifu na taarifa zake zipo ndani ya Jeshi la Polisi.

Alisema,Haule ameshafanya matukio kadhaa ya uhalifu ndani ya ofisi za CCM na ushahidi upo wazi ndiyo maana amechukua jukumu la kumpiga marufuku kufika hapo.

" Huyu kijana amekua akifanya mambo mbalimbali yanayokichafua Chama ikiwemo kujifanya mmoja ya maofisa wa CCM Wilaya kwa maslahi yake binafsi," alisema Mfaume.

"Mimi ndiye Katibu wa CCM Wilaya ninawajibu wa kulinda maslahi ya ofisi za Chama na mali zake siwezi kukubali kuona mtu anafanya vitendo visivyo na maadili nikafumbia macho, nimemfukuza Haule kwa sababu hana jukumu lolote ndani ya ofisi zetu lakini pia tabia zake za kihalifu zinajulikana kila mahali ikiwemo ndani ya vyombo vya dola,"alisema Mfaume.

Kuhusu suala la kumtishia maisha alisema,ni jukumu la mlalamikaji kwenda Polisi kufungua kesi kama ana uthibitisho wa kutosha na yuko tayari kujibu tuhuma hizo.



Mkuu wa Wilaya ya Moshi Godfrey Mnzava amefanya ziara katika Kijiji cha Umbwe Kati, Kata ya Kibosho Magharibi, Tarafa ya Kibosho, na kutatua mgogoro wa muda mrefu uliohusiana na ubainishaji wa barabara.

Mgogoro huo ulitokana na baadhi ya wananchi kutokubaliana na ubainishaji wa barabara uliofanywa na Kamati ya Maendeleo ya Kata. Kutokana na hilo palitokea kutokuelewana kuhusu mipaka halisi ya barabara hiyo.

Katika ziara hiyo Mnzava alisikiliza pande zote zinazohusika. Kwa kushirikiana na wananchi na viongozi wa eneo hilo alisimamia zoezi la ubainishaji wa mipaka ya barabara. Uamuzi huo ulikubaliwa na wananchi wenye maeneo yanayopitiwa na barabara, ambao walikubali kuachia eneo hilo kwa ajili ya matumizi ya umma.

Barabara hiyo inatumika na wananchi kufika Kituo cha Afya cha Umbwe. Inasaidia pia katika shughuli nyingine za kiuchumi na kijamii katika eneo hilo.

Akizungumza na wananchi baada ya zoezi hilo, Mnzava amewataka kuendelea kudumisha umoja, amani na mshikamano. Amesema maendeleo ya jamii yanategemea wananchi kuweka mbele maslahi ya pamoja.

Wananchi wa Umbwe Kati wamesema wameridhika na jinsi mgogoro huo umetatuliwa na wameahidi kushirikiana na viongozi katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.





Na Janeth Raphael - MichuziTv

Tanzania na Misri zimefikia makubaliano ya kuimarisha ushirikiano katika sekta za kilimo na mifugo, hatua inayotarajiwa kufungua ukurasa mpya wa uwekezaji kupitia maendeleo ya Ranchi ya Ruvu na matumizi ya teknolojia za kisasa katika uzalishaji wa chakula.

Akizungumza Ikulu jijini Dar es Salaam, Julai 18, 2026, baada ya mazungumzo rasmi na Rais wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri, Abdel Fattah El-Sisi, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, alisema nchi hizo mbili zimekubaliana kuongeza ushirikiano ili kuinua uzalishaji wa mazao na mifugo na kuimarisha usalama wa chakula.

Rais Samia amesema mazungumzo yao yalijikita katika namna ya kutumia teknolojia za kisasa za umwagiliaji na ufugaji ili kuongeza tija, huku yakifungua fursa mpya za uwekezaji katika sekta hizo muhimu kwa uchumi wa nchi.

Ameeleza kuwa bara la Afrika bado linatumia fedha nyingi kuagiza chakula kutoka nje, jambo linalosisitiza umuhimu wa kuongeza uzalishaji wa ndani kwa kutumia rasilimali zilizopo na kuwekeza katika kilimo chenye tija.

Aidha, Rais Samia amesema Tanzania ina zaidi ya hekta milioni 29 zinazofaa kwa kilimo cha umwagiliaji, hali inayoweka mazingira mazuri kwa uwekezaji mkubwa katika uzalishaji wa chakula kwa ajili ya soko la ndani na nje ya nchi.

Katika hatua nyingine, amesema Serikali ya Misri imeonesha nia ya kushirikiana na Tanzania kuendeleza Ranchi ya Ruvu, ambayo kwa sasa haijatumika kikamilifu, kwa lengo la kuifanya kuwa kitovu cha uzalishaji wa kisasa wa mifugo na uwekezaji wa pamoja.

Rais Samia pia amewahamasisha wawekezaji kutoka Misri kushirikiana na taasisi za Serikali zenye maeneo makubwa ya uzalishaji, ikiwemo Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Magereza, Shirika la Taifa la Ranchi (NARCO), pamoja na miradi ya kilimo inayotekelezwa Zanzibar.

Amesisitiza kuwa ushirikiano huo unalenga kuongeza uzalishaji wa chakula, kuvutia uwekezaji, kuzalisha ajira kwa Watanzania na kuiwezesha Tanzania kuwa kitovu cha uzalishaji wa mazao na mifugo kwa soko la Afrika na masoko mengine ya kimataifa.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri, Mhe. Abdel Fattah El-Sisi, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 18 Julai Juni, 2026.


Na Janeth Raphael - MichuziTv

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema Tanzania na Misri zimefikia makubaliano ya kuimarisha ushirikiano katika sekta ya usafirishaji wa baharini kwa kuunganisha bandari za mataifa hayo mawili, hatua inayolenga kuongeza biashara, kuvutia uwekezaji na kupanua masoko ndani ya Afrika na ukanda wa Ghuba.

Akizungumza Ikulu, Dar es Salaam, Julai 18, 2026, baada ya mazungumzo rasmi na Rais wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri, Abdel Fattah El-Sisi, Rais Samia alisema ushirikiano huo utahusisha maendeleo ya Bandari ya Dar es Salaam pamoja na ujenzi wa eneo maalumu la kuhifadhi bidhaa na makontena ya Misri katika Bandari ya Bagamoyo, ambalo litaunganishwa na reli hadi Kwala ili kuongeza ufanisi wa usafirishaji wa mizigo.

Amesema pande zote mbili zimekubaliana kuendeleza mazungumzo ya kuunganisha Bandari za Dar es Salaam, Bagamoyo, Safaga pamoja na bandari nyingine za Misri, jambo litakalorahisisha usafirishaji wa bidhaa, kupunguza gharama za biashara na kuongeza ushindani wa mataifa hayo katika soko la kimataifa.

Kwa mujibu wa Rais Samia, mpango huo utafungua njia kwa bidhaa za Tanzania kuingia kwa urahisi zaidi katika masoko ya nchi za Ghuba, huku bidhaa kutoka Misri zikipata fursa ya kufikia nchi za Afrika Mashariki na Kusini kupitia bandari za Tanzania.

Katika kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi, Rais Samia amesema Rais El-Sisi ameambatana na ujumbe wa wafanyabiashara wakubwa 35 wanaoshiriki Jukwaa la Biashara Tanzania na Misri, hatua inayotarajiwa kuongeza kiwango cha biashara na uwekezaji kati ya mataifa hayo mawili.

Aidha, amesema Shirika la Ndege la EgyptAir tayari linaendesha safari tatu kwa wiki kati ya Misri na Tanzania, huku akiihimiza Air Tanzania kuanzisha safari za moja kwa moja kuelekea Misri ili kurahisisha usafiri wa abiria, kukuza utalii na kuongeza fursa za biashara.

Rais Samia amesisitiza kuwa ushirikiano huo unaipa Tanzania nafasi ya kuendelea kuwa kitovu muhimu cha biashara na usafirishaji kwa ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini, huku ukiimarisha zaidi uhusiano wa kiuchumi na kibiashara kati ya Tanzania na Misri.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri, Mhe. Abdel Fattah El-Sisi wakati wakishuhudia utiaji saini wa Mikataba na Hati za Makubaliano katika sekta ya umeme, nishati jadidifu, pamoja na masuala ya mbalimbali za Uchukuzi baina ya Tanzania na Misri. Hafla hiyo ilifanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 18 Julai, 2026.






Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongoza Ujumbe wa Tanzania kwenye mazungumzo rasmi na Ujumbe wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri, uliongozwa na Rais wa nchi hiyo, Mhe. Abdel Fattah El-Sisi, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 18 Julai Juni, 2026.

Na Victor  Masangu, Pwani

Hatimaye Chama cha wafanyakazi wa serikali na afya  (TUGHE) Mkoa wa Pwani kimefanya uchaguzi wake mkuu na kuweza kumchangua kwa kishindo Mwenyekiti  aliyekuwa anatetea  kiti  chake  Catherine Katele ambaye ameweza kuibuka na ushindi baada ya   kupata kura 33 dhidi ya mpinzani wake ambaye amejinyakulia kura zipatazo 18 kati ya kura halali 51 ambazo zimepigwa.

Katika uchaguzi huo ambao  ulifanyika  katika ukumbi wa Mkuu  wa Mkoa wa Pwani ulihudhuliwa na wajumbe mbali mbali kutoka Wilaya zote saba za Mkoa wa Pwani zikiwemo, Kibaha, Rufuji, Bagamoyo , Mkuranga, Mafia,Kisarawe, pamoja na Kibiti ulikuwa na amani na utulivu katika kipindi chote cha uendeshaji wa  zoezi  zima la upigaji wa kura.    

Akitangaza matokeo hayo msimamizi wa uchaguzi ambaye pia ni  Afisa kazi   Mkoa wa Pwani Metta Nahonyo  amesema kwamba uchaguzi umekwanda vizuri bila ya kuwa na dosari ya aina yoyote na kwamba wagombea wote wamekubalina na matokeo ambayo yametokea na kuongeza kuwa  fomu zote wameweza kuzisahi  bila shaka ya yoyote ikiwa ni ishara tosha ya kuridhika na matokeo hayo.

Msimamizi huyo  amebainisha kwamba katika kinyang'anyiro cha uchaguzi huo Mwenyekiti ambaye ambaye alikuwa anapambana kukitetea kiti chake Catherine Katele ameweza kuibuka mshindi kwa  kupata kura za halali zipatazo 33 huku mpinzani wake Ivo Ndukeki ameweza kupata kura za halali zipatazo 18.

"Nikiwa kama msimamizi wa uchaguzi huu wa Tughe Mkoa wa Pwani nimeweza kusimamia vizuri mwenendo mzima wa zoezi hili  la uchaguzi na ninashukuru Mungu kwamba zoezi hili limemalizika salama bila ya kuwa na kosaro ya aina yoyote ile na wagombea wotte wamekubaliana na matokeo ambayo yametokea kwani uchaguzi ulikwenda vizuri  na kila mgombea  ameridhika na ameweza kusaini fomu ,"amebainisha Msimamizi huyo.

Kwa upande wake  Mwenyekiti wa TUGHE Mkoa wa Pwani ambaye  ndiye alikuwa akitetea kiti hicho kwa mara nyingine amewashukuru kwa dhati wajumbe wote wa Mkutano mkuu wa kuweza kumuanmini kumchagua tena kwa mara nyingine na kwamba ataendelea kuwapa ushirikiano wa hali na mali katika  kukijenga chama bila kuwa na ubaguzi wowote,

Mwenyekiti huyo amesema kwamba kwa sasa mikakti ambayo amejiwekea ni kuweza kuimarisha  nguvu kazi katika sula zima la kuwatetea wafanyakazi katika kulinda maslahi yao na kwamba atakuwa nao bega kwa bega ili kuweza kuleta chachu ya maendelea katika nyanja mabali mbali mbali,

Pia hakusita kuelezea jinsi gani atakavyoweza kuwa na mipango madhubuti ya kuendelea kukiimarisha chama kuanzia ngazi za chini hadi Mkoa ikiwa pamoja na kutafuta fursa za kiuchumi  katika Wilaza zote za Mkoa wa Pwani na kuahidi kuwasaidia watu wenye ulemavu ili waweze kujikomboa.\

Mwenyekiti huyo amemshukuru na kumpa pomgeza Rais wa awamu ya Sita Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kuweza kusimama imara kwa kutenga fedga nyingi ambazo zimeleta matokeo chanya katika kutekeleza miradi mbali mbali ya maendeleo .  

Katibu wa TUGHE Mkoa wa Pwani Jonas Rwegoshora amewapongeza viongozi wote ambao wamemeza kuchaguliwa katika mkutano huo na kwamba ataendelea kushirikiana nao bega kwa bega kwa ajili ya mashali mapana ya chama hicho.

Nao baadhi ya wagombea katika uchaguzi huo wamesema kwamba kwa sasa wataweza tofauti zao pembeni na kuungana kwa pamoja na viongozi wote ambao wamechaguliwa kwa lengo la kudumisha upendo amani na na kuleta chachu ya maendelea kwa maslahi ya watu wote hususan wanachama wa Tughe Mkoa wa Pwani na Taifa kwa ujumla.

 Katika uchaguzi mbali na kumchagua Mwenyekiti wameteuliwa wajumbe wa  nafasi mbali mbali ikiwemo nafasi za wawakilishi wa vijana, wawakilishi wa walemavu, pamoja na wajumbe wengine ambao wataweza kuwakilisha  katika ngazi za  Mkoa na Taifa katika mikutano mbali mbali.





Na George Maziku, Kahama
 
DIWANI wa Kata ya Majengo, Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, wilayani Kahama, mkoa wa Shinyanga Shida Zacharia Soko amechangia chakula chenye thamani ya zaidi ya milioni 6 kwa ajili ya wanafunzi wanaosoma kwenye shule tatu zilizopo kwenye kata yake.
 
Chakula hicho amekitoa juzi katika mkutano wa wazazi wa wanafunzi wanaosoma katikà shule tatu za Mama Samia Sekondari, shule ya msingi Anderson Msumba na shule ya msingi Majengo.
 
Mkutano huo aliuitisha yeye mwenyewe kwa lengo la kuwahasisha wazazi kuchangia chakula kwa ajili ya watoto wao, ambapo mgeni rasmi alikuwa Mkuu wa wilaya ya Kahama Frank Nkinda. 
 
Diwani huyo alitoa gunia 45 za mahindi yenye thamani ya milioni 2925000, maharage kilogramu 600 zenye thamani ya Sh. milioni 1200000, Mchele kilogramu 600 zenye thamani ya 12000, na sukari kilogramu 600  zenye thamani ya Sh. 1200000.

Akitoa mchanganuo wa mchango huo wakati akiukabidhi kwa Mkuu wa Wilaya, diwani Soko alisema kila shule itapata gunia 15 za mahindi, kilogramu 200 za maharage, kilogramu 200 za mchele na kilogramu 75 za sukari.

"Mheshimiwa mkuu wetu wa wilaya hapa mbele yako kuna pakeji (package) tatu ya chakula kwa ajili ya watoto wa shule ya sekondari ya Mama Samia, mimi ni mzee wa pakeji tu, hayo ndio mapigo yangu. Pakeji kama hii nimetoa kwa shule mbili za msingi za Anderson Msumba na Majengo", alifafanua Soko.

Akipokea mchango huo, mkuu wa wilaya Nkinda alimpongeza diwani  Soko kwa moyo wake wa kujitolea na kumtaka aendelee na moyo huo wa huruma na kujali wanyonge.

"Nakupongeza sana mheshimiwa diwani kwa moyo wako wa kutoa kwa wanyonge, wewe unaweza kufikiri haya unayofanya kuwa mambo madogo lakini nataka nikuambie kuwa haya ni mambo makubwa sana, ninakuomba uendelee na moyo huo na Mungu atakulipa", alisema mkuu wa wilaya Nkinda.

Aliongeza kuwa, " Nami nakuunga mkono kwa kuchangia kilogramu 500 za mahindi ambazo nitazitoa leo hii baada ya zoezi hili la kupokea mchango wako", alibainisha Nkinda.

Mkuu huyo wa wilaya alitoa wito kwa wazazi na wadau wengine wa maendeleo kuunga mkono juhudi za diwani Soko kwa kuchangia kwa wingi chakula cha watoto wao wanaosoma katikà shule hizo.

Diwani Soko amekuwa na utaratibu wa kuchangia chakula kwa wanafunzi wanaosoma katika shule tatu za kata yake tangu achaguliwe kushika wadhifa huo katika uchaguzi mkuu wa Oktoba, 2025.

Wakitoa maoni yao baadhi ya wazazi waliohudhuria mkutano huo waliunga mkono mpango wa kuchangia chakula cha wanafunzi ili kuwasaidia watoto kufuatilia vizuri masomo kutoka kwa walimu wao.
" Ni jambo zuri sana kwasababu itawasaidia watoto wetu kusoma kwa utulivu na kuelewa wanachofundishwa na walimu wao. Mimi nitachangia na ninawashauri wazazi wenzangu kuchangia kwa ajili ya ustawi wa watoto wetu", alisema Zuhura Rashid Salum ambaye ni mzazi wa mwanafunzi anaesoma shule ya msingi Majengo.

Naye Diana James aliyejitambulisha kuwa mzazi wa mwanafunzi anaesoma shule ya msingi Anderson Msumba alikubaliana na Mpango huo na kuahidi kuchangia.

"Mpango huu ni mzuri na muhimu sana kwasababu njaa ni mbaya, mtoto mwenye njaa hawezi kuzingatia kikamilifu masomo yake, hata sisi watu wazima hatuwezi kufanya kazi tukiwa na njaa, Mimi nipo tayari kuchangia chakula kwa mtoto wangu", alisema mzazi huyo.

Mkuu Wa Wilaya ya Kahama Mkoani Shinyanga Frank Nkinda akiwa katikà mkutano wa  hadhara wa wazazi ulioitishwa na diwani Wa Kata ya Majengo Zacharia shida Soko
Magunia 15 ya Mahindi yaliyotolewa na diwani Soko kwaajili ya Chakula katikà shule ya Sekondari Samia iliyopo Kata ya Majengo Manispaa ya kahama

Wazazi Wa wanafunzi Wa shule tatu zilizopo katikà Kata ya Majengo
Diwani Wa kata ya Majengo Zacharia SOKO akifuatilia hotuba ya mkuu Wa wilaya
 



Na Mwandishi Wetu
TAASISI ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), imezindua mfumo wa kidijitali wa usajili wa wagonjwa na teknolojia mpya ya kisasa ya Dozee ya kufuatilia hali ya mgonjwa hata kiwa nyumbani.

Uzinduzi huo ulifanyika jana jijini Arushwa ambapo mgeni rasmi alikuwa Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini,Paul Makonda.

Alisema uwekezaji huo unaifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zinazoendelea kupiga hatua barani Afrika katika matumizi ya ubunifu wa kidijitali kuboresha huduma za matibabu na kutekeleza malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Makonda alisema matumizi ya teknolojia katika usajili wa wagonjwa, utunzaji wa kumbukumbu za kitabibu na ufuatiliaji wa wagonjwa baada ya matibabu ni sehemu ya maono ya Serikali ya kujenga taifa lenye uchumi unaotegemea maarifa, sayansi na teknolojia.

Katika kambi hiyo, Taasisi ya Moyo Mfumo wa teknolojia unaojulikana kitaalamu kama Dozee, una uwezo wa kufuatilia hali ya mgonjwa kwa wakati halisi akiwa amelazwa hospitalini au baada ya kuruhusiwa kurejea nyumbani.

Dozee ni mfumo unaotumia kifaa maalumu kinachowekwa chini ya godoro la mgonjwa na kufuatilia viashiria muhimu vya afya bila kulazimika kuunganisha vifaa vingi moja kwa moja kwenye mwili wake.

Dkt. Kisenge alisema mfumo huo una uwezo wa kufuatilia viashiria muhimu vya afya vya mgonjwa, vinavyojulikana kitaalamu kama vital signs, ikiwemo mapigo ya moyo, kiwango cha oksijeni kwenye damu na shinikizo la damu.

Alisema taarifa zinazokusanywa kupitia mfumo huo zinaweza kumfikia daktari kwa njia ya kidijitali, ikiwemo kupitia simu ya mkononi, hivyo kumwezesha kufuatilia mwenendo wa afya ya mgonjwa hata akiwa nje ya hospitali au anaendelea na shughuli nyingine.

Alifafanua kuwa teknolojia hiyo imelenga kusaidia kupunguza vifo vinavyoweza kuzuilika, hususan vinavyotokea baada ya hali ya mgonjwa kubadilika ghafla akiwa nyumbani baada ya kuruhusiwa kutoka hospitalini.

“Mara nyingi wagonjwa wanaporuhusiwa kwenda nyumbani, hali zao zinaweza kubadilika ghafla. Shinikizo la damu linaweza kushuka, mapigo ya moyo yanaweza kwenda kwa kasi sana au kiwango cha oksijeni kwenye damu kikapungua. Kupitia teknolojia hii, daktari anaweza kupata taarifa kwa wakati na kuchukua hatua mapema kabla hali ya mgonjwa haijawa mbaya,” alisema Dkt. Kisenge.

Alisema mfumo huo hautawanufaisha wagonjwa wa moyo na waliopata huduma za upasuaji pekee, bali unaweza pia kutumika kuwafuatilia wagonjwa wenye matatizo mengine ya kiafya.

Alitolea mfano wagonjwa wenye malaria kali, ambao wanaweza kupata mabadiliko ya ghafla ya mapigo ya moyo, shinikizo la damu na kiwango cha oksijeni kwenye damu.

Kwa mujibu wa Dkt. Kisenge, kufuatiliwa kwa viashiria hivyo kwa wakati kunaweza kuwasaidia wataalamu wa afya kubaini hatari mapema, kumfuata mgonjwa alipo, kumrudisha hospitalini inapohitajika na kumpatia matibabu sahihi.

Alisema uwekezaji katika mfumo huo unaifanya JKCI kuwa miongoni mwa taasisi zinazoongoza katika matumizi ya teknolojia za kisasa za kufuatilia wagonjwa, huku akieleza kuwa teknolojia ya aina hiyo inatumika pia katika nchi zikiwemo India na Marekani.

Dkt. Kisenge alisema mafanikio hayo yametokana na uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha huduma za afya za kibingwa na ubingwa bobezi nchini.



Top News