KAMATI ya  Bunge ya kudumu ya Bajeti imeipongeza Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA)kwa kuanzisha kitengo maalumu kwa ajili ya walipakodi wakubwa hatua ambayo imechangia ongezeko la kodi inayokusanywa na mamlaka hiyo.

Aidha Kamati hiyo imewatoa hofu wananchi juu ya dhana ya uwepo wa upendeleo wa kutolipa kodi kwa walipa kodi wakubwa ikisisitiza kuwa kila mwenye wajibu wa kulipa kodi kwa Mamlaka hiyo analipa kulingana na kiwango kile kile anachostahili.

Akizungumza wakati wa ziara ya kamati hiyo kutembelea kitengo cha walipa kodi wakubwa Jijini Dar es Salaam Mei 30, 2026 Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mashimba Ndaki amesema kuboreshwa kwa mazingira  na kufanya kuwa kama 'faragha' kwa mlipa kodi mkubwa kumewavutia wengi na hivyo kufanya mapato kupaa.

"Kwa namna hali ilivyo, ni tofauti na miaka miwili iliyopita, Sasa hivi walipa kodi wakubwa wanachangia asilia 40 ya Kodi tunayoikusanya, hiki ni kiwango kikubwa ambacho msingi wake Mkuu ni kuboreshwa kwa mazingira kulikofanywa na TRA kwa hili tunawapongeza sana" amesema Mashimba.

Pamoja na hilo amesema TRA imepiga hatua kubwa kwa kuboresha huduma mbalimbali ikiwemo ya watumishi wake kuwa na lugha nzuri jambo linalowavutia wananchi wengi kulipa kodi kwa hiari tofauti na ilivyokuwa zamani ambapo Mamlaka hiyo ilikuwa ikiogopeka.

Kuhusu dhana ya upendeleo kwa walipa kodi wakubwa, Ndaki amesisitiza kuwa hilo siyo jambo la kweli na ndiyo maana walipa kodi hao wameweza kuchangia asilimia 40 ya kodi yote iliyokusanywa huku walipa kodi wengine wakichangia asilimia 60 zilizobaki.

Kwa upande wake Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Yusuph Juma Mwenda ameshukuru hatua ya Kamati ya Bunge kuzitembelea Mamlaka hiyo akidai kuwa ziara hiyo itazidi kuwahamasisha kuendelea kuboresha huduma zao.

Amesema TRA itaendelea kutenda haki kwa walipa kodi wote kwa kuzingatia madaraja yao  kwa yule anastahili kulipa kikubwa atalipa kikubwa, anayestahili kulipa kidogo atalipa kidogo na yule asiyestahili kulipa hatolipa kwa kuwa hiyo ndiyo utaratibu wa utendaji wa Mamlaka hiyo.

Amesema uwepo wa Ofisi hiyo kwa ajili ya walipa kodi wakubwa wakiwemo wenye makampuni mbalimbali zaidi ya 851 ambao wamechangia asilimia 40 sawa na Trilioni 14 ya kodi iliyokusanywa  Mwaka huu ni kielelezo tosha cha kuwa walipa kodi wakubwa wanalipa kodi.




 

▪️︎ Aagiza watumishi waliohusika na ubadhirifu wa zaidi ya shilingi milioni 500 Manyoni wakamatwe na fedha zirudishwe

▪️︎ Akemea rushwa, wizi wa fedha za umma na matumizi mabaya ya madaraka

▪️︎ Aonya viongozi wanaowaza vyeo badala ya kutatua changamoto za wananchi


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba ameagiza watumishi waliohusishwa na ubadhirifu wa zaidi ya shilingi milioni 500 katika Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni watafutwe popote walipo, wakamatwe na kuchukuliwa hatua za kisheria na kinidhamu huku fedha hizo zikirejeshwa serikalini.

"Wamechota fedha za wananchi. Watafutwe hata ambao walishahamishwa, popote walipo wakamatwe, wawekwe ndani na fedha za Serikali zirudi. Hii si fedha ya mtu binafsi, ni fedha ya wananchi," alisema Dkt. Mwigulu.

Dkt. Mwigulu ametoa agizo hilo leo Jumamosi Mei 30, 2026 alipozungumza na wananchi wa Wilaya ya Manyoni katika Viwanja vya Tambukareli mkoani Singida akiwa katika ziara ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo, kusikiliza na kutatua changamoto za wananchi.

Alisema taarifa alizopokea zinaonesha kuwa jumla ya zaidi ya shilingi milioni 501 zilichotwa kutoka akaunti mbalimbali za halmashauri ikiwemo Akaunti ya Maendeleo (zaidi ya shilingi milioni 213), Akaunti ya Amana (zaidi ya shilingi milioni 259) na Akaunti ya Mapato ya Ndani (zaidi ya shilingi milioni 42), jambo ambalo haliwezi kuvumiliwa na Serikali.

Waziri Mkuu aliwataja watumishi wanaodaiwa kuhusika katika ubadhirifu huo kuwa ni aliyekuwa Mweka Hazina wa Halmashauri hiyo Mwakapala, ambaye kwa sasa amehamishiwa mkoani Songwe, Mhasibu wa Mapato Edward Kilungu na Eliamini Maliki.

Aidha, alimwagiza Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida (RPC) kuhakikisha watumishi hao wanatafutwa, wanakamatwa na kuwekwa mahabusu hadi fedha za Serikali zitakapopatikana.

"Mweka Hazina Mwakapala arudishwe, Edward Kilungu na Eliamini Maliki watafutwe. Wakamatwe, wawekwe ndani na wasitoke mpaka fedha ya Serikali irudi," alisema Dkt. Mwigulu.

Aidha, Waziri Mkuu alimuagiza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI kuhakikisha watumishi wote waliohusika wanasimamishwa kazi mara moja huku taratibu za kinidhamu na kisheria zikiendelea.

"Barua za kuwasimamisha kazi zitoke leo leo na hatua zinazostahili za kiutumishi zifanyike haraka. Wasitoke mpaka fedha za wananchi zirudi," alisema.

Sambamba na hilo, Dkt. Mwigulu alikemea vitendo vya rushwa, ubadhirifu wa mali za umma na matumizi mabaya ya madaraka, akieleza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita haitamvumilia mtu yeyote atakayehujumu rasilimali za wananchi.

"Ninachukia uvivu, uzembe, wizi na kuonewa kwa wanyonge. Nitawashikisha adabu wezi, walaghai na wote wanaotumia nafasi zao kuwaumiza wananchi," alisema.

Aidha, alimpongeza Mkuu wa Mkoa wa Singida pamoja na vyombo vya Serikali kwa kugundua na kuanza kuchukua hatua dhidi ya ubadhirifu huo.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu alikemea tabia ya baadhi ya viongozi kutumia muda mwingi kufikiria uchaguzi na vyeo badala ya kutatua changamoto za wananchi, akisisitiza kuwa Watanzania wanahitaji maendeleo na huduma bora zaidi kuliko siasa za makundi.

"Watanzania wana kiu ya maendeleo. Kiu waliyonayo si ya kugawana madaraka, bali ni maendeleo na kuondoka kwa kero zinazowakabili katika maisha yao ya kila siku," alisema.

Aliongeza kuwa viongozi wanapaswa kutumia nafasi walizopewa kutatua matatizo ya wananchi badala ya kutumia muda mwingi kufuatilia nafasi nyingine za uongozi.

"Kila mmoja afanye kazi katika nafasi aliyopewa. Watanzania wana shida nyingi zinazohitaji ufumbuzi na si siasa za makundi au mbio za madaraka," alisema.

Pia, Waziri Mkuu alisema Serikali itaendelea kusimamia haki za wananchi, kuimarisha uwajibikaji katika utumishi wa umma na kuhakikisha fedha za maendeleo zinafika na kutumika kwa malengo yaliyokusudiwa.

Alisema Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kutekeleza hatua mbalimbali za kuboresha maisha ya wananchi ikiwemo kutoa elimu bila ada kwa Kidato cha Tano na Sita, Programu ya Samia Scholarship na kuondoa riba kwa mikopo ya elimu ya juu kwa wahitimu ambao hawajapata ajira.

Aidha, alieleza kuwa Serikali imeendelea kutekeleza miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo Mradi wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere, Reli ya Kisasa (SGR), miradi ya maji, afya, barabara na usambazaji wa umeme vijijini ili kuharakisha maendeleo na kuboresha huduma kwa wananchi.

Waziri Mkuu aliwahakikishia wananchi wa Manyoni na Watanzania kwa ujumla kuwa Serikali itaendelea kutatua changamoto zinazowakabili na kusimamia kikamilifu utekelezaji wa miradi ya maendeleo ili kuhakikisha matunda ya maendeleo yanawafikia wananchi wote.

"Niwahakikishie Watanzania kwamba yote yaliyomo kwenye Ilani na ahadi za Mheshimiwa Rais yataendelea kutekelezwa kwa manufaa ya wananchi," alisema.












- zaidi ya Sh milioni 126 zaokolewa katika kipindi cha miezi sita

- huduma za upatikanaji wa hewa tiba zaimarika katika hospitali ya mawenzi

- Zaidi ya Mitungi 3000 ya Oksijeni imezalishwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mawenzi katika kipindi cha miezi sita tangu mradi huo uanze kufanya kazi , hali iliyosaidia kuondoa changamoto ya upatikanaji wa hewa tiba katika hospitali hiyo.

Hayo yamebainishwa leo na Mganga Mfawidhi wa hospitali hiyo, Dk Abdillah Issah alipokuwa akisoma taarifa ya ya mradi huo mbele ya Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Kenani Kihongosi alipotembelea na kukagua mradi huo.

Akizungumza baada ya kusomewa taarifa ya mradi na kutembelea sehemu mbalimbali za mradi huo Kihongosi amesema mradi huo ni miongoni mwa uwekezaji mkubwa uliofanywa na serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa lengo la kuboresha huduma za afya kwa wananchi wa Kilimanjaro na maeneo jirani.

Kihongosi amesema kabla ya kusimikwa kwa mtambo huo hospitali ilikuwa ikikabiliwa na gharama kubwa za ununuzi na usafirishaji wa oksijeni kutoka nje ya mkoa, hali iliyokuwa ikiathiri ufanisi wa utoaji wa huduma.

“Kupitia uwekezaji huo, hospitali imefanikiwa kupunguza gharama za uendeshaji, kuimarisha huduma za wagonjwa mahututi na kuongeza uwezo wa kusambaza oksijeni katika vituo vingine vinavyohitaji huduma hiyo,” amesema kihongosi.

Katika hatua nyingine amewapongeza viongozi na watumishi wa hospitali hiyo kwa usimamizi mzuri wa huduma, akisisitiza mafanikio hayo yanaonesha namna serikali inavyoendelea kuboresha sekta ya afya na kusogeza huduma bora karibu na wananchi.

Awali akisoma taarifa ya mradi huo Dk Issah amesema mradi huo umegharimu jumla ya Sh bilioni 1.94 na katika kipindi cha miezi sita tangu mradi kuanza kufanya kazi mitungi 3,313 ya Oksijeni imezalishwa katika hospitali hiyo, hali iliyisaidia kuondoa changamoto ya upatikanaji wa hewa tiba.

Pia ameongeza kuwa hatua hiyo imesaidia hospitali hiyo kuokoa takribani Sh milioni 126 katika kipindi cha miezi sita baada ya kuanza kutumia mtambo wa kuzalisha hewa tiba ya oksijeni.

“Hatua hiyo imepunguza utegemezi wa ununuzi wa oksijeni kutoka kwa wazabuni wa nje na kuimarisha utoaji wa huduma za afya katika hospitali ya Mawenzi,” amesema Dk Issah.








WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali imeweka mazingira wezeshi kwa ajili ya kukuza uchumi wa viwanda na kuongeza thamani ya mazao ya kilimo, huku akiwataka vijana, sekta binafsi na wawekezaji kutumia fursa zilizopo kuanzisha viwanda vya kuchakata korosho na mazao mengine ya kilimo.

“Serikali haipaswi kufanya jukumu hilo peke yake la kujenga viwanda. Lakini kwa kuwa zao hili halikuwa zao la asili lililozoeleka kwa Mkoa wa Singida, ni lazima hatua za aina hii ziweze kufanyika. Baada ya hapo vijana na sekta binafsi wachukue jukumu hilo la kutengeneza viwanda vya kutosha vya kubangua korosho zinazozalishwa hapa Mkoa wa Singida na pengine hata mikoa mingine,” alisema Dkt. Mwigulu.

Dkt. Mwigulu amesema hayo leo Jumamosi Mei 30, 2026 alipokagua Mradi wa Mnyororo wa Thamani wa Korosho kupitia Kiwanda Darasa cha Kubangua Korosho (KIDAKUKO) cha CAMARTEC kilichopo Masigati wilayani Manyoni, akiwa katika ziara ya kikazi mkoani Singida.

Waziri Mkuu aliwapongeza wananchi wa Manyoni kwa kuendelea kuimarisha kilimo cha korosho na kuwa miongoni mwa maeneo yaliyoanzisha kwa mafanikio zao hilo katika Mkoa wa Singida.

“Niwapongeze ndugu zetu wa Manyoni kwa kuanza kuwa wa kwanza kulima zao hili la korosho kwa Mkoa wa Singida. Hongereni sana, mmetupandisha chati wote,” alisema.

Alisema zao la korosho ni miongoni mwa mazao mbadala yenye umuhimu mkubwa katika kuimarisha uchumi wa wananchi na taifa kutokana na mabadiliko yanayoendelea kujitokeza katika masoko ya mazao mbalimbali duniani.

“Kuna mazao ambayo zamani yalikuwa yanafanya vizuri sana duniani, lakini yanaendelea kupata changamoto. Kadri tunapopata changamoto katika zao moja, lazima tuwe na mazao mbadala mengi. Sasa kwa Manyoni imeanza vizuri hili zao la korosho,” alisema.

Aidha, Dkt. Mwigulu alisema Kiwanda Darasa hicho kinaendana na utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kujenga uchumi wa kisasa unaotegemea uzalishaji, viwanda, teknolojia na uwekezaji wa sekta binafsi.

Awali, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Kituo cha Zana za Kilimo na Teknolojia Vijijini (CAMARTEC), Mhandisi Godfrey Mwinama, alimweleza Waziri Mkuu kuwa Kiwanda Darasa cha Kubangua Korosho (KIDAKUKO) cha Masigati kilijengwa kwa gharama ya shilingi milioni 637.5 na kilizinduliwa rasmi Septemba 30, 2025.

Mhandisi Mwinama alisema kiwanda hicho ni miongoni mwa jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuhakikisha matokeo ya tafiti na ubunifu wa ndani yanawanufaisha wananchi kupitia uzalishaji, uchakataji na kuongeza thamani ya mazao ya kilimo.

Alisema kiwanda hicho kilianzishwa kwa lengo la kutoa mafunzo ya ubanguaji na uchakataji wa korosho kwa vijana, wanawake na wawekezaji, huku kikiwa na uwezo wa kufundisha watu 50 kwa wakati mmoja.

Aidha, alisema kiwanda hicho kina uwezo wa kubangua kati ya tani 1.36 hadi tani 2.72 za korosho kwa siku kulingana na kiwango cha uzalishaji na uzoefu wa wabanguaji.

“Teknolojia nyingi zinazotumika katika kiwanda hiki zimeundwa hapa nchini. Zipo mashine za kubangua korosho, makaushio, vifaa vya uchambuzi wa korosho na mifumo mingine ya uchakataji iliyobuniwa na wataalamu wa CAMARTEC,” alisema Mhandisi Mwinama.

Kwa upande wake, mwakilishi wa Bodi ya Korosho Tanzania Ray Mtangi alisema Serikali imeendelea kuimarisha mnyororo wa thamani wa zao la korosho kupitia huduma za ugani, pembejeo za ruzuku, ushirika wa wakulima, maghala ya kuhifadhi mazao na mifumo ya kisasa ya uuzaji wa korosho.

Taarifa ya CAMARTEC ilieleza kuwa endapo korosho zote zinazozalishwa nchini zitachakatwa hapa nchini, zaidi ya ajira 36,458 zinaweza kuzalishwa sambamba na kuongeza mapato ya wananchi na thamani ya bidhaa zitokanazo na zao hilo.









-Wahifadhi wa Sao Hill wavutiwa na mafanikio ya utalii ikolojia, watakiwa kuhamasisha kura za Tuzo za Kimataifa za Utalii



Na Mwandishi Wetu, Pwani


Hifadhi ya Msitu wa Asili ya Pugu Kazimzumbwi mkoani Pwani imeendelea kujidhihirisha kuwa moja ya hazina kubwa za utalii wa ikolojia nchini baada ya kuvutia wahifadhi kutoka Shamba la Miti Sao Hill waliotembelea eneo hilo kujifunza mbinu za uhifadhi, usimamizi wa bioanuai na maendeleo ya utalii endelevu.

Ziara hiyo imekuja wakati Tanzania ikiendelea kuimarisha juhudi za kuhifadhi rasilimali za misitu na kuendeleza utalii wa asili kama sehemu ya kuongeza mchango wa sekta hiyo katika uchumi wa taifa, huku Pugu Kazimzumbwi ikitajwa kuwa miongoni mwa maeneo yanayoongoza kwa kuhifadhi urithi wa kihistoria na mazingira ya kipekee karibu na Jiji la Dar es Salaam.

Wakati wa ziara hiyo, wahifadhi hao walitembelea vivutio mbalimbali vinavyopatikana ndani ya hifadhi hiyo ikiwemo misitu ya asili yenye bioanuai adimu, njia za utalii wa kutembea msituni, maeneo ya kihistoria pamoja na vivutio vya kiikolojia vinavyovutia watalii wa ndani na nje ya nchi.

Maofisa wa hifadhi hiyo waliwaeleza wageni hao kuhusu hatua zinazochukuliwa kulinda mazingira, kudhibiti shughuli zinazohatarisha misitu na kuendeleza utalii wa ikolojia unaochochea maendeleo ya jamii na kuongeza mapato ya taifa bila kuathiri mfumo wa ikolojia.

Akizungumza baada ya kutembelea vivutio hivyo, Kiongozi wa Msafara huo, CO I Donald Makupa, alisema uzoefu walioupata katika Hifadhi ya Msitu wa Asili ya Pugu Kazimzumbwi utakuwa chachu ya kuboresha mikakati ya uhifadhi katika maeneo wanayoyasimamia.

“Tumeshuhudia namna ambavyo uhifadhi wa misitu unaweza kwenda sambamba na maendeleo ya utalii. Maarifa haya yatatusaidia kuimarisha usimamizi wa rasilimali za misitu na kuongeza thamani ya maeneo yetu ya uhifadhi,” alisema Makupa.

Aliongeza kuwa ushirikiano na kubadilishana uzoefu kati ya taasisi na maeneo mbalimbali ya uhifadhi ni nyenzo muhimu katika kuhakikisha sekta ya misitu na utalii inaendelea kukua kwa manufaa ya taifa.

Kwa upande wake, Afisa Utalii wa Hifadhi ya Msitu wa Asili ya Pugu Kazimzumbwi, Mbaruku Sinon, alisema ujio wa wahifadhi hao unaonesha namna maeneo ya uhifadhi yanavyozidi kuwa vituo vya kujifunzia na kubadilishana uzoefu kuhusu mbinu bora za kulinda mazingira na kuendeleza utalii.

Alisema kuimarika kwa ushirikiano kati ya wahifadhi kutoka maeneo mbalimbali kutasaidia kuongeza ubunifu katika usimamizi wa rasilimali za misitu, kukuza idadi ya watalii na kuhakikisha bioanuai inayopatikana nchini inalindwa kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

“Pugu Kazimzumbwi ni zaidi ya hifadhi ya misitu. Ni darasa la uhifadhi, kituo cha utalii wa ikolojia na sehemu inayobeba historia muhimu ya nchi yetu. Tunahitaji kuendelea kushirikiana ili kuitangaza zaidi ndani na nje ya Tanzania,” alisema Sinon.

Katika ziara hiyo, wahifadhi hao walikumbushwa umuhimu wa kushiriki kampeni ya kuhamasisha wananchi kupigia kura vivutio vya utalii vinavyosimamiwa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), hususan Pugu Kazimzumbwi Nature Forest Reserve na Amani Nature Forest Reserve, ambavyo vimeingia katika kinyang’anyiro cha Tuzo za Kimataifa za Utalii.

Wadau wa uhifadhi wanaamini kuwa mafanikio ya maeneo hayo katika tuzo hizo yataongeza mwonekano wa Tanzania katika soko la utalii duniani, kuvutia wageni wengi zaidi na kuchochea uwekezaji katika utalii wa asili unaozingatia uhifadhi wa mazingira.

Kwa miaka ya karibuni, Pugu Kazimzumbwi imeendelea kuwa kivutio muhimu kwa watalii, wanafunzi, watafiti na wadau wa mazingira kutokana na utajiri wake wa bioanuai, historia ya kipekee na ukaribu wake na Jiji la Dar es Salaam, hali inayoiweka katika nafasi ya kuwa moja ya nguzo muhimu za utalii wa ikolojia nchini.




WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba leo (Jumamosi, Mei 30, 2026) akiwa katika ziara ya kikazi mkoani Singida amekagua maendeleo ya utekelezaji wa Mradi wa Uboreshaji Huduma ya Maji wa Mji wa Manyoni unaotekelezwa kwa gharama ya shilingi bilioni 28 na unaotarajiwa kuhudumia wakazi zaidi ya 64,667.

Akipokea taarifa ya utekelezaji wa mradi huo kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Manyoni (MAUWASA), Mhandisi Lucas Mwinuka, Dkt. Mwigulu alielezwa kuwa mradi huo umefikia asilimia 80 ya utekelezaji na unatarajiwa kukamilika Agosti 10, 2026.

Mhandisi Mwinuka alisema mradi huo unatekelezwa na Serikali kupitia Wizara ya Maji na unahusisha uchimbaji wa visima vya maji, ujenzi wa kituo cha kusukuma maji, ujenzi wa tanki lenye uwezo wa kuhifadhi lita milioni mbili za maji pamoja na ulazaji wa mabomba ya kusambaza maji kwa wananchi.

Alisema mradi huo utakapokamilika utaongeza uzalishaji wa maji kutoka wastani wa lita milioni 2.057 kwa siku hadi lita milioni 6.48 kwa siku na hivyo kuongeza upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama kwa wakazi zaidi ya 64,667 wa mji wa Manyoni.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Maji, Mhandisi Kundo Andrea Mathew alisema mradi huo ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi na juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama.

Mhandisi Kundo alisema mradi wa Manyoni ni sehemu ya kifurushi cha nne cha Mradi wa Miji 28 unaotekelezwa katika miji ya Kiomboi, Singida, Manyoni, Chamwino, Chemba na Mugumu kwa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni 142. Alisema kukamilika kwa miradi hiyo kutaimarisha upatikanaji wa maji safi na salama, kuchochea shughuli za kiuchumi na kuimarisha ustawi wa wananchi katika maeneo hayo.

Alisema kukamilika kwa mradi huo kutasaidia kuongeza upatikanaji wa maji katika Mji wa Manyoni kutoka asilimia 49 ya sasa hadi asilimia 100 na kuweka msingi wa kukidhi mahitaji ya maji kwa zaidi ya miaka 20 ijayo kutokana na ukuaji wa mji na ongezeko la idadi ya watu.

Aidha, alisema Serikali imeanza hatua za kuhifadhi maeneo ya vyanzo vya maji ili kuhakikisha upatikanaji endelevu wa huduma hiyo sambamba na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.












Na Said Mwishehe,Michuzi TV


KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) Dk.Asha-Rose Migiroameweka wazi kuwa vurugu zilizotokeaOktoba 29 mwaka 2025 zimetia doa katikataifa la Tanzania lakini limeweza kuvukakipindi kile na kubaki kuwa Taifa moja.

Dk.Migiro ameyasema hayo alipokuwa ajibu maswali ya mtangazaji wa Crown Media Salim Kikeke aliyekuwa akifanya mahojiano maalumu na Katibu Mkuu huyo kuhusu hali ambayo Taifa limepitia baada ya vurugu za Oktoba29.

Katika swali lake Kikeke alisema kuna watu kutoka vyama vya vingine na wengine kutoka ndani ya CCM wanazungumza mambo ambayo ukiyatazama unaona kimsingi kama yanaligawa Taifa badala ya kulileta pamoja, hivyo akataka kujua msimamo wa Chama Cha Mapinduzi katika hilo

“Pamoja na kwamba wapo wanaopazasauti hizo lakini ukweli ni tumebaki kuwataifa moja, tumeendeelea kuendeshashughuli zetu za kiuchumi na kijamii bilakutetereka ndani muda mfupi,amani ilirejea,uchumi wetu bado umebaki tulivu natunajua duniani kuna vyombo vya kupima,kutathimini ukuaji wa uchumi.

Vyombo vyote vimeeleza hata baada ya kadhia ile ya Oktoba 29 uchumi wetu umebaki tulivu.

“Hii inaonesha sio tu ustahimilivu ,inaonesha tumeendeelea kuwa taifa mojatukiwa na njia moja ya kujijenga kijamii nakiuchumi lakini utaona hali hii ya umoja nautulivu haipimwi tu na sisi wa ndani au Chama Cha Mapinduzi .Tumeona baada yatukuo lile bado watu wameendelea kuwa naimani na taifa hili, wameendeelea kuonautulivu wetu umerejea.”

Akiendelea kujibu Dk.Migiro amesema Rais na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi aliwapokea wawekezaji kutoka mataifa matano.Pia taifa limepokea wafanyabiashara kutoka Urusi huku akiongeza China pia imeendelea kuwekeza.

“Nasiku za karibuni Mwakillishi Mkazi wa Kanda hii wa Benki ya Dunia alikwenda kumuaga Rais wetu baada ya kumaliza kipindi chake cha utumishi katika kanda hiina alimueleza kuwaTanzania bado inamaoteo mazuri ya kukua kwa uchumi.

“Kwahiyo siamini kama tungekuwa ni taifalililogawanyika haya yote yangetokea nawapo tumewasikia wanaosema taifalimegawanyika ,limepasuka.Chochote wanachokiona ambacho ni kiashiria cha kugawanyika au kiashiria cha mpasuko Mtanzania yeyote ambaye ana mapenzi mema na taifa letu atakuwa na sauti ya kuunganisha ,sio sauti ya kuleta mpasuko na hili linakuwa na umuhimu zaidi kwa watukama sisi viongozi .

“Nimewahi kuwa kiongozi kwa nafasi yangundogo mpaka ngazi ya Uwaziri. Kitaifanimepata heshima kubwa ya kufanya kazinyingine katika taifa letu ,nilikuwa mpaka Julai mwaka jana nilipata heshima ya kuwa Mwenyekiti wa Tume ya kitalaam ya uandishi wa Dira ya Taifa 2050 .Niheshima kubwa na ni sehemu ya uongozi ambaonilipata heshima ya kuwa nayo.

“Kwa maana hiyo ninapozungumza lazimakauli yangu iakisi dhamana na heshimaniliyopewa ya kuwa kiongozi .Sauti yangukama kiongozi au viongozi wengine wawewakijamii , dini au kisiasa. Kiongozi wakweli ni yule anayepaza sauti ya kukubalikuna kitu kilitupata lakini kusema kwamba tusiendelee kukaa kwenye kadhia hii kwa namna ya kuendeleza mpasuko,”amesema Dk.Migiro na kusisitiza hakuna mgawanyiko.

Pia amesema viongozi wanawajibu wakuhakikisha wanaendelea kwa kauli zetu navitendo vyao kushikamana kama taifa nakuimarisha umoja wetu .

Kuhusu ripoti ya Jaji Chande kuwa walibainiuwepo wa picha za akili unde ambazozilitizamwa na kuna madai pengine kunapicha zinasingiziwa akili unde ili kufichayaliyotokea Oktoba 29 na nini maoni yaCCM

Dk.Migiro amejibu kuna picha ambazo akiliunde lakini kuna picha ambazo ni za matukio ya zamani zimeunganishwa namatukio ya Oktoba 29 na tume imeelezaziko picha ambazo ni za matukio yasehemu nyingine nje ya nchi lakinizimeunganishwa.

“Sasa tume ilipokuwa inaeleza metholodojia iliyotumia ilisema \wametumia watalaam wautambuzi kutambua zile picha ni za lini ,zawapi na za wakati gani. Hayo ni masuala yakitalaam .Mimi na wewe ndugu Kikekesidhani kama tuna nafasi kubwa yakuzungumzia utalaam wa aina hii.

“Wewe mwenzangu ni mtalaam wa mambo ya habari kama hivi unavyonihoji .Mimi ninataaluma yangu ndogo ya sheria lakini sikusomea sheria ya utambuzi .Nadhani itakuwa vema na busara tukawaachia watalaam wakachambua hili na tunaamini baada ya Tume ya Upelelezi wa Jinai kumaliza kazi yake tutapata mwanga zaidi kuonesha mambo zaidi yalikuaje Oktoba 29 na baadae nini kilitokea,”amesemaDk.Migiro.


Paris, Ufaransa

Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Ufaransa, Mheshimiwa Saidi Othman Yakubu, amekutana na ujumbe wa viongozi wanawake 18 kutoka Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) waliopo nchini Ufaransa kwa ziara ya kitaaluma ya kujenga uwezo na kubadilishana uzoefu kuhusu uongozi, usimamizi wa taasisi za elimu ya juu na maendeleo ya wanawake katika nafasi za maamuzi.

Ujumbe huo unaongozwa na Dkt. Janeth Emanuel Kigoba, Mkuu wa Kitivo cha Elimu cha Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, ambaye pamoja na viongozi wengine wanashiriki programu mbalimbali za kujifunza na kutathmini mifumo bora ya uongozi na utawala katika taasisi za elimu ya juu.

Akizungumza na ujumbe huo katika Ubalozi wa Tanzania mjini Paris, Balozi Yakubu alisema imekuwa jambo la kutia moyo kuona kuwa sekta ya elimu ya juu, ambayo kwa miaka mingi imekuwa nyuma katika kufikia usawa wa kijinsia ikilinganishwa na baadhi ya sekta nyingine, sasa inaendelea kupiga hatua na kuongeza ushiriki wa wanawake katika nafasi za uongozi.

“Nimefarijika kuona idadi kubwa ya wanawake viongozi kutoka taasisi ya elimu ya juu wakishiriki katika programu za kujijengea uwezo. Elimu ndiyo msingi wa maendeleo ya jamii, hivyo ni muhimu kuona wanawake wakichukua nafasi zao stahiki katika kuongoza taasisi hizi muhimu,” alisema Balozi Yakubu.

Aliongeza kuwa vyuo vikuu vina nafasi ya kipekee katika kuandaa viongozi, wataalamu na watunga sera wa kesho, hivyo kuwepo kwa usawa wa kijinsia katika sekta hiyo kuna mchango mkubwa katika kuharakisha maendeleo ya taifa na jamii kwa ujumla.

Balozi Yakubu aliwahimiza washiriki hao kuendelea kuwa vinara wa mabadiliko katika taasisi zao kwa kuhakikisha kuwa wanawake wengi zaidi wanapata fursa za kushiriki katika uongozi, utafiti na ufundishaji.

Kwa upande wake, Dkt. Janeth Emanuel Kigoba alimshukuru Balozi Yakubu na Ubalozi wa Tanzania nchini Ufaransa kwa mapokezi na ushauri walioutoa kwa ujumbe huo, akisisitiza kuwa ziara hiyo imewapa washiriki fursa muhimu ya kujifunza uzoefu wa kimataifa unaoweza kusaidia kuimarisha utendaji na uongozi wa taasisi za elimu ya juu nchini Tanzania.

Ziara hiyo ni sehemu ya juhudi za Chuo Kikuu Huria cha Tanzania za kuimarisha uwezo wa viongozi wanawake na kukuza ushiriki wao katika nafasi za juu za uongozi, sambamba na kuchochea maendeleo ya elimu ya juu na usawa wa kijinsia nchini.



Na Mwandishi wetu Dodoma

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Dodoma imefichua kasoro nzito katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo, ikiwemo ujenzi wa mabweni ya Shule ya Sekondari ya Wasichana Kibaigwa wilayani Kongwa, ambapo baadhi ya kazi zimeonekana kutotekelezwa kwa viwango vilivyokubaliwa kwenye mikataba ya Serikali.

Katika taarifa yake kwa waandishi wa habari leo jijini Dodoma kuhusu utekelezaji wa shughuli za TAKUKURU kwa kipindi cha Januari hadi Machi 2026, Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Dodoma, Christopher Myava, amesema taasisi hiyo imebaini matumizi ya nyavu kwenye madirisha na sehemu za hewa za milango badala ya vioo vilivyotakiwa kuwekwa kwa mujibu wa ramani ya ujenzi.

Amesema uchunguzi uliofanywa na TAKUKURU umeonesha pia kuwa baadhi ya vyoo vya mabweni hayo havikuwekewa masinki kama ilivyoelekezwa kwenye michoro ya mradi, huku kuta zikikosa vigae vilivyopangwa kufungwa kwa mujibu wa makubaliano ya utekelezaji wa kazi hiyo.

“Tumebaini tofauti kubwa kati ya kazi iliyotekelezwa na maelekezo yaliyopo kwenye mkataba wa mradi. Haya ni mambo ambayo yanaathiri ubora wa miradi pamoja na thamani ya fedha za Serikali,” amesema Myava.

Mbali na dosari hizo, TAKUKURU imeeleza kuwa baadhi ya vitasa vilivyowekwa kwenye mabweni hayo havifanani na vile vilivyoainishwa kwenye mkataba, huku baadhi ya vifaa vya ujenzi ikiwemo matofali na mabati vikidaiwa kutowasilishwa maabara kwa ajili ya kupimwa ubora wake kabla ya kutumika kwenye mradi.

Katika hatua nyingine, Myava amesema taasisi hiyo imefanikiwa kubaini mapungufu katika jumla ya miradi 36 ya maendeleo yenye thamani ya zaidi ya Shilingi bilioni 156.4 kupitia operesheni za ufuatiliaji zilizofanywa katika sekta mbalimbali mkoani Dodoma.

Amesema TAKUKURU itaendelea kusimamia kwa karibu utekelezaji wa miradi yote ya maendeleo ili kuhakikisha fedha za umma zinaleta matokeo yaliyokusudiwa na wananchi wanapata huduma bora kutokana na uwekezaji wa Serikali.

“Lengo letu ni kuona miradi yote inakamilika kwa viwango vinavyostahili na kuhakikisha hakuna mianya ya ubadhirifu wa fedha za umma,” ameongeza.

Baada ya kubaini dosari hizo, wahusika wa miradi hiyo wamepewa maelekezo ya kurekebisha mapungufu yote yaliyojitokeza ili miradi hiyo iweze kukidhi viwango vya kitaalamu pamoja na thamani ya fedha zilizotumika.


NA DENIS MLOWE,NJOMBE.

MAANDALIZI ya mbio za Uchumi Parachichi Marathon yameanza kushika kasi katika mkoa wa Njombe, ikiwa ni tukio kubwa lenye lengo la kutangaza na kuhamasisha thamani ya zao la parachichi ambalo ni uti wa mgongo wa uchumi wa wakazi wa Nyanda za Juu Kusini.

Marathon hii, inayotarajiwa kufanyika tarehe 26 Julai 2026 katika viwanja vya Sabasaba Njombe Mjini, imeandaliwa kwa lengo mahususi la kuonyesha mchango wa zao la parachichi katika kujenga uchumi imara wa mkoa huo kupitia zao la Parachichi.

Kupitia mbio hizi, wakulima wadogo watapatiwa elimu kuhusu kilimo bora, namna ya kuongeza uzalishaji, pamoja na kuwezeshwa kupata pembejeo, mbolea na vifaa vya kisasa vya kilimo.

Akizungumza kuhusu maandalizi hayo, Mkurugenzi wa Speak Sports Games Promotion, Respicius Mtabingwa Kajura, ambaye pia ndiye msimamizi mkuu wa tukio hilo, amesema mbio hizo ni zaidi ya mashindano ya mbio ni jukwaa la uchumi, elimu na fursa kwa jamii.

Amesema kuwa tukio hili ni bonanza kubwa kuwahi kutokea katika mikoa ya Nyanda za Juu Kusini na linatarajiwa kuvutia washiriki kutoka maeneo mbalimbali ndani na nje ya nchi.

Kajura amesema kuwa mbio hizo zitakuwa na makundi tofauti ya washiriki wakiwemo wanaokimbia 42km, 21km, 10km na 5km. Aidha, kaulimbiu ya mwaka huu, Parachichi ni Uchumi wa Njombe na Lishe Bora ya Mwanao, inalenga kuhimiza matumizi ya parachichi kama zao la lishe na biashara.

Ametoa wito kwa wadau wa michezo, kilimo, afya na jamii kwa ujumla kuungana nao ili kufanikisha tukio hilo ambalo lina matarajio ya kuleta hamasa na utalii wa michezo katika mkoa wa Njombe.

Mkurugenzi Kajura amewakaribisha wananchi wote kutoa ushauri, mawazo na michango yao ili kuhakikisha Uchumi Parachichi Marathon inafanyika kwa ubora na mafanikio makubwa kama inavyotarajiwa.


Benki ya NMB imeendelea kuimarisha huduma kwa wafanyabiashara kupitia NMB Business Club, jukwaa linalowapa wateja elimu ya fedha, teknolojia na fursa mbalimbali za kukuza biashara zao kwa uendelevu. Semina hiyo imefanyika katika Ukumbi wa Cardinal Rugambwa, Dar es Salaam.

Akizungumza katika semina hiyo, Mwenyekiti wa NMB Business Club Mkoa wa Dar es Salaam na Mjumbe wa Bodi ya Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania (JWT), Award Mpandila, alisema jukwaa hilo limekuwa muhimu kwa kuwaunganisha wafanyabiashara na kuwajengea uwezo wa kutumia mifumo rasmi ya kifedha.

 Aliwahimiza wafanyabiashara kupitisha mauzo yao kupitia benki ili kujenga historia nzuri ya kifedha inayoweza kuwasaidia kupata huduma mbalimbali, ikiwemo mikopo.

Kwa upande wake, Meneja Mwandamizi wa Business Banking Benki ya NMB, Reynold Tony, alisema benki hiyo itaendelea kutoa bidhaa, elimu na suluhisho zinazolenga kuimarisha biashara za wateja wake. Alisema NMB inalenga kuwa mshirika wa karibu wa wafanyabiashara katika kujenga biashara imara na zinazoweza kukabiliana na mabadiliko ya soko.

Baadhi ya wafanyabiashara waliohudhuria, akiwemo Eileen Kunaga na Ally Kuburi kutoka Ilala, walisema jukwaa hilo limewasaidia kupata elimu kuhusu matumizi ya sola, usimamizi wa fedha na huduma za taasisi mbalimbali, ikiwemo TRA. Walisema maarifa hayo yanaweza kupunguza gharama za uendeshaji na kusaidia biashara kukua kwa muda mrefu.
Mwenyekiti wa NMB Business Club Mkoa wa Dar es Salaam na Mjumbe wa Bodi ya Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania (JWT), Awadhi Mpandila, akizungumza wakati wa semina ya NMB Business Club iliyofanyika Dar es Salaam. Walioketi meza kuu ni Reynold Tony Lusingu, Meneja Mwandamizi wa Idara ya Biashara Benki ya NMB; William Nkuna, Kaimu Meneja wa Kanda ya Dar es Salaam; Petro Kyando, Katibu wa NMB Business Club; na Leah Mwakang’ata, Mkuu wa Idara ya Amana za Biashara (kulia) wa Benki ya NMB.
Mkuu wa Idara ya Amana za Biashara Benki ya NMB, Leah Mwakang’ata, akizungumza wakati wa semina ya NMB Business Club iliyofanyika Dar es Salaam. Walioketi meza kuu ni Reynold Tony, Meneja Mwandamizi wa Idara ya Biashara Benki ya NMB; William Nkuna, Kaimu Meneja wa Kanda ya Dar es Salaam; Awadhi Mpandila, Mwenyekiti wa NMB Business Club Mkoa wa Dar es Salaam; na Petro Kyando, Katibu wa NMB Business Club.





















Top News