📍Awataka viongozi wa dini kuhubiri Umoja na mshikamano

NA MWANDISHI WETU, MBEYA

MKUU wa Wilaya ya Mbeya, Mhe. Solomon Itunda, ametoa wito kwa viongozi wa dini na jamii kwa ujumla kuimarisha vita dhidi ya mmomonyoko wa maadili, huku akisisitiza kuwa wanawake ni nguzo muhimu katika kulea kizazi chenye nidhamu na uzalendo nchini.

Mhe. Itunda ametoa kauli hiyo Jumamosi, Februari 28, 2026, alipomwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Beno Malisa, katika ufunguzi wa Kongamano la Kitaifa la Wanawake wa Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT) lililofanyika katika ukumbi wa VETA jijini Mbeya.

Akihutubia washiriki wa kongamano hilo waliotoka katika mikoa zaidi ya 13 nchini, DC Itunda alisema Serikali ya Awamu ya Sita inatambua mchango wa kipekee wa wanawake katika kulinda misingi ya amani, maadili na hofu ya Mungu, mambo ambayo ni chemchemi ya ustawi wa Taifa.

"Wanawake ni nguzo ya Taifa. Serikali inaendelea kuthamini ushirikiano na taasisi za kidini katika kukuza maadili na kuchochea maendeleo. Ni wajibu wenu kuendelea kuwa chachu ya mabadiliko chanya kwa kusimamia malezi na kupinga kwa nguvu zote vitendo vinavyovunja heshima ya jamii yetu," alisisitiza Mhe. Itunda.

Pia aliwataka viongozi wa dini pamoja na kusimamia mmomonyoko wa maadili lakini pia amewaasa kuhakikisha wanahubiri amani ya nchi, upendo na mshikamano na kuwaunga mkono viongozi nchini.

Asifu Falsafa ya 4R ya Rais Samia

Katika hatua nyingine, Mhe. Itunda alimpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa uongozi wake uliotukuka unaopambanuliwa na falsafa ya 4R (Maridhiano, Ustahimilivu, Mageuzi na Ujenzi Mpya).

Alibainisha kuwa kupitia falsafa hiyo, Rais Samia amefanikiwa kuliunganisha Taifa, kuimarisha maridhiano kati ya makundi mbalimbali na kujenga mazingira ya amani yanayowezesha mikutano mikubwa kama hiyo ya CCT kufanyika kwa utulivu.

"Falsafa ya 4R imekuwa dira yetu katika kujenga mshikamano wa kitaifa na kuvumiliana. Mkoa wa Mbeya utaendelea kuwa kitovu cha makongamano yenye tija kutokana na ushirikiano mkubwa uliopo kati ya Serikali na taasisi za kidini," alisema.

Viongozi wa Dini Waimwagia Sifa Serikali

Kwa upande wao, viongozi wa dini waliohudhuria kongamano hilo wameishukuru Serikali kwa kuendelea kuweka mazingira rafiki ya kuabudu na kufanya shughuli za kijamii.

Kongamano hilo limehitimishwa kwa maombi maalum ya kuliombea Taifa, viongozi wa Serikali na kuliombea Kanisa ili liendelee kuwa nuru ya maadili nchini.

Viongozi waliohudhuria ni pamoja na Askofu wa Dayosisi ya Konde (KKKT), Baba Askofu Gefrey Mwaihaba, Katibu Mkuu wa CCT, Mchungaji Canon Dkt. Moses Matonya, pamoja na Maaskofu wa Makanisa ya Anglikana na Moravian (Jimbo la Mbeya).







Maafisa Ushirika wa vyama vya ushirika nchini wametakiwa kutumia ipasavyo elimu na maarifa waliyoyapata katika mafunzo maalum ili kuwa chachu ya mafanikio, uwajibikaji na maendeleo endelevu ndani ya vyama vya ushirika.

Akifunga rasmi mafunzo ya wiki mbili ya kuwajengea uwezo maafisa hao katika masuala ya usimamizi wa vyama, Mrajisi Msaidizi anayeshughulikia Uhamasishaji, Masoko na Uwekezaji amesema mafunzo hayo yamekuwa nyenzo muhimu katika kuimarisha ufanisi wa vyama vya ushirika, hususan katika ngazi za mikoa na kusisitiza kuwa mafunzo hayo yamewapa washiriki mbinu za kisasa za uongozi, usimamizi na ushirikishaji wanachama, hatua itakayosaidia kuongeza tija, uwazi na ushindani katika soko.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Isaiah Kapakala, alisema mafunzo hayo yalilenga pia kuwajengea washiriki uelewa mpana juu ya matumizi sahihi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), akibainisha kuwa matumizi ya teknolojia ni nguzo muhimu katika kuongeza ufanisi na uwajibikaji wa taasisi za ushirika katika zama za sasa.

Naye mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo, Sophia Kagimbo, amesema mafunzo hayo yamewapa msukumo mpya wa kufanya kazi kwa ubunifu, weledi na kujituma zaidi, akiahidi kuwa watatumia maarifa waliyoyapata kuhakikisha vyama vya ushirika vinapiga hatua kubwa za maendeleo kote nchini.

Mafunzo hayo ni sehemu ya mkakati wa kuimarisha sekta ya ushirika nchini ili iwe injini ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii.






Na Diana Byera,Kyerwa

MKUU wa Wilaya ya Kyerwa mkoani Kagera Zaituni Msofe, amekabidhi rasmi nyumba kwa familia ya Jenifer Richard mwenye uhitaji maalum Mkazi wa Kakerere katika Kata ya Nkwenda iliyojengwa.

Nyumba hiyo imejengwa na Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Kagera, Devotha Daniel Mburarugaba ikiwa ni sehemu ya juhudi zake za kusaidia wananchi wenye uhitaji maalum.

Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano, Msofe amemshukuru Mbunge kwa kugusa maisha ya wananchi kwa vitendo, akielez hatua hiyo ni mfano wa kuigwa katika kuimarisha mshikamano na utu kwa jamii.

“Ninawapongeza viongozi wanaotumia nafasi zao kuleta matumaini kwa wananchi. Nawahimiza watu wote wenye uwezo kujitokeza kuwasaidia wasiojiweza katika jamii yetu,” amesema Mkuu wa Wilaya Msofe.

Kwa upande wake, Mbunge Devotha Daniel Mburarugaba amesema aliguswa kuanza ujenzi wa nyumba hiyo baada ya kuona picha Mjongeo kupitia mitandao ya kijamii akiwa katika mazingira magumu ya maisha.

“Nilipoona hali aliyokuwa nayo, niliguswa na nikachukua hatua ya haraka. Leo tunashuhudia matokeo ya mshikamano na upendo,” amesema Mbunge huyo.

Aidha, Mbunge ameahidi pamoja na ujenzi wa nyumba hiyo, atahakikisha anakata bima ya afya kwa wote kwa familia yote ili kuwawezesha kupata huduma za matibabu kwa uhakika na kwa wakati.

Hata hivyo Mbunge Devotha Mburarugaba pia amempongeza Raisa Dk.Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuweka mazingira mazuri yanayowezesha viongozi kuwahudumia wananchi na kusimamia maendeleo ya watu wenye mahitaji maalum.

Kwa niaba ya familia, ndugu wa karibu wametoa shukrani za dhati kwa Mbunge na uongozi wa Wilaya ya Kyerwa kwa msaada huo mkubwa ambapo wamefafanua walikuwa wanaishi katika mazingira magumu kwa muda mrefu.

Hivyo nyumba hiyo ni mwanzo mpya wa maisha yao na imewarejeshea matumaini na heshima katika jamii. Walimuombea Mbunge na viongozi wote waliohusika baraka na mafanikio katika kuendelea kuwahudumia wananchi.







MKUU wa Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga Peter Masindi, amesema kulipa kodi ni muhimu sana kwa maendeleo ya Taifa kwani kupitia Kodi Serikali imeendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika jamii.

Ameyasema hayo hivi karibuni wakati alipotembelewa na Maafisa wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Ofisini kwake Wilayani Kishapu kwa lengo la kumjuulisha juu ya uwepo wa zoezi la elimu ya kodi mlango kwa mlango wilayani humo.

Masindi, amesema kupitia kodi Serikali imeendelea kuimarisha miundombinu mbalimbali na hatimae kuboresha huduma za kijamii.

"Ukilipa kodi ndio unajenga barabara, shule, hospitali, unachangia uwepo wa huduma za maji na miradi ya kimkakati kama Treni ya Mwendokasi (SGR)" amesema Masindi.

Aidha, ameipongeza TRA kwa kuendelea kukusanya kodi kwa mafanikio huku akitolea mfano wa kuvunja kwa rekodi ya makusanyo kwa kila mwezi kwa TRA Shinyanga na maeneo mbalimbali nchini Tanzania.

Mbali na hayo, amewapongeza wafanyabiashara wa Kishapu kwa kuendelea kulipa kodi kwa hiari huku akisisitiza TRA kuendelea na urasimishaji wa Wafanyabiashara kwani utaongeza wingi wa mapato na hatimae kuboresha huduma za kijamii kadri zinavyohitajika.

Pamoja na hayo, ameiomba TRA kuweka Ofisi ya Huduma za Kikodi Wilayani Kishapu kwani kukosekana kwa Ofisi katika Wilaya hiyo kunasababisha changamoto kwa walipakodi.

"Tunahitaji Ofisi ifunguliwe (Kishapu) kwa ajili ya kuwarahisishia walipakodi kuendelea kulipa kodi kwa hiari, kwani kwa sasa wananchi wanatembea umbali mrefu kwa ajili ya kuzifuata huduma za kikodi" amesema Mhe. Masindi.

Kwa Upande wake, Afisa Msimamizi wa Kodi mkoa wa Shinyanga Semeni Mbegi kwa niaba ya Kiongozi wa timu hiyo amesema katika kipindi cha takriban wiki moja wameweza kutembelea zaidi ya wafanyabiashara 2000 kwa kuwapatia elimu na kusikilza changamoto zao.

Amefafanua kuwa katika zoezi hilo wamebaini mambo mbalimbali ikiwemo baadhi ya wafanyabiashara kufanya biashara bila ya kujisajili TRA, baadhi ya wafanyabiashara biashara zao bado hawajakadiriwa, na baadhi yao hawatumii mashine za EFD ipasavyo.

Semeni ametoa wito kwa wafanyabiashara kuhakikisha wanasajili biashara zao, wanakadiriwa na kulipa kodi ya awamu kwa wakati ili kuiwezesha Serikali kukamilisha miradi ya maendeleo kwa wakati.








RUVUMA | Februari 28, 2026


Katibu Mkuu wa TRAMEPRO Atoa Wito wa Kugeuza Historia ya Vita vya Maji Maji kuwa Fursa za Maendeleo
Katibu Mkuu wa Shirika la Tiba Asili na Uhifadhi wa Mazingira (TRAMEPRO), Boniventura Mwalongo, leo Februari 28, 2026, amesema kuwa historia ya mashujaa wa Vita vya Maji Maji inapaswa kuenziwa kwa vitendo kwa kuigeuza kuwa chachu ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Mashujaa wa Vita vya Maji Maji yaliyofanyika Mkoa wa Ruvuma, Mwalongo alisema kuwa mashujaa hao walionesha ujasiri, umoja na uzalendo wa hali ya juu katika kupigania ardhi, heshima na utu wa Mwafrika.

“Damu ya mashujaa wa Vita vya Maji Maji ndiyo mbegu ya uhuru wetu. Ni wajibu wetu kuhakikisha historia yao haiishii kwenye kumbukumbu pekee, bali inakuwa sehemu ya maendeleo ya kizazi cha sasa na kijacho,” alisema Mwalongo.

Alisisitiza kuwa maadhimisho hayo yanapaswa kutumika kama jukwaa la kuhamasisha uwekezaji katika utalii wa kihistoria, tafiti za kisayansi pamoja na matumizi ya teknolojia katika kuhifadhi makumbusho na nyaraka muhimu za kihistoria.

“Tunaweza kugeuza maeneo ya kihistoria kuwa vivutio vya utalii, tukafungua ajira kwa vijana wetu na kuimarisha uchumi wa mkoa wetu. Hii ndiyo njia bora ya kuwaenzi mashujaa wetu,” aliongeza.

Aidha, aliwataka wadau mbalimbali kushirikiana katika kuhifadhi mazingira na kuendeleza tiba asili kama sehemu ya kulinda na kuenzi urithi wa taifa.

Maadhimisho ya Siku ya Mashujaa wa Vita vya Maji Maji Mkoa wa Ruvuma yameendelea kuwa kumbukumbu muhimu ya historia ya mapambano dhidi ya ukoloni, huku yakihamasisha kizazi cha sasa kujivunia utamaduni na urithi wao.

“Mashujaa wetu, tunawaenzi leo na milele,” alihitimisha Mwalongo.





 



Wananchi mbalimbali pamoja na baadhi ya viongozi wamepata fursa ya kutembelea onyesho maalum la Nduna Mkomanile lililofanyika katika Kituo cha Baraza la Wazee wa Mila na Desturi Mkoa wa Ruvuma.

Onyesho hilo limefanyika tarehe 27/02/2026, likiwakutanisha wadau mbalimbali waliotaka kujifunza na kutambua mchango wa wanawake katika historia ya ukombozi wa taifa.

Nduna Mkomanile anatambulika kama mwanamke shujaa, muhamasishaji na muwajibikaji katika jamii yake, aliyesimama imara wakati wa Vita vya Majimaji kupigania uhuru dhidi ya utawala wa kikoloni.

Lengo la onyesho hilo lilikuwa kuangazia mchango wa wanawake katika harakati za ukombozi dhidi ya wakoloni na kuonesha namna ambavyo mchango wao unaendelea kuonekana hata katika jamii ya sasa.

Onyesho hilo lilikuwa sehemu ya matukio ya Tamasha la Kumbukizi ya Vita vya Majimaji na Utalii wa Utamaduni, lililoratibiwa na Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Makumbusho ya Taifa kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma pamoja na Baraza la Wazee wa Mila na Desturi.

Kupitia onyesho hilo, wananchi wamepata nafasi ya kujifunza historia ya shujaa Nduna Mkomanile, namna alivyoshiriki katika Vita vya Majimaji na mapambano dhidi ya utawala wa kikoloni, pamoja na jukumu lake la kusambaza dawa wakati wa vita. Aidha, wamefahamu umaarufu wake, nafasi yake ya uongozi na ushauri, pamoja na mchango wake katika kuratibu mawasiliano wakati wa mapambano hayo.

Utafiti wa taarifa na maandalizi ya onyesho la Nduna Mkomanile yamewezeshwa na Women Fund Tanzania kupitia mtandao wa Kestoria, ikiwa ni muendelezo wa kampeni yao ya kuhakikisha historia za wanawake zinaibuliwa, zinaandikwa, zinatambuliwa na kusambazwa kwa kizazi cha sasa na kijacho.




















Meneja wa Ufungaji wa Mgodi wa Barrick Buzwagi, Mhandisi Zonnastraal Mumbi akitoa maelezo kwa Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Wallace Karia na ujumbe wake walipotembelea kituo cha michezo cha Buzwagi.

Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Wallace Karia na ujumbe wake wakitembelea maeneo mbalimbali ya kituo cha michezo cha Buzwagi.

Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Wallace Karia na ujumbe wake wakitembelea maeneo mbalimbali ya kituo cha michezo cha Buzwagi.

Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Wallace Karia na ujumbe wake wakitembelea maeneo mbalimbali ya kituo cha michezo cha Buzwagi.

Baadhi ya wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Taifa wa shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) wakiwa katika picha ya pamoja na Rais wa shirikisho hilo Wallace Karia na Meneja wa Ufungaji wa Mgodi wa Barrick Buzwagi, Mhandisi Zonnastraal Mumbi.


**

Mgodi wa Barrick Buzwagi ambao uko katika mchakato wa kufungwa kwa kushirikiana na Serikali umepongezwa kwa kuweka miundombinu ya kituo cha michezo ambacho kitasaidia kukuza mchezo wa soka na michezo mingineyo nchini.

Pongezi hizo zimetolewa na Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Wallace Karia, alipoongoza wajumbe wa Mkutano Mkuu wa taifa wa shirikisho hilo kutembelea eneo hilo ambapo amesema miundombinu iliyopo inaridhisha.

Amesema miundombinu hiyo kuanzia nyumba za malazi kwa wanamichezo, viwanja vya michezo, usalama, pamoja na mazingira yake kwa ujumla ipo katika hali nzuri na inakidhi mahitaji ya kuanzishwa kwa kituo hicho.

“Natoa shukrani kwa kampuni ya Barrick na Serikali kwa kukubali ombi la kuanzishwa kituo cha michezo katika eneo la mgodi uliofungwa, tunafurahi kuona kituo kiko katika hali nzuri na kina viwango vikubwa kwa ajili ya kuhudumia wanamichezo, hii ni fursa muhimu kwa maendeleo ya michezo yetu”, amesema.

Kwa upande wake Mjumbe wa Kamati Tendaji ya Taifa ya TFF, Azan Mufti, amesema kutengwa kwa eneo hilo kwa ajili ya wanamichezo kunadhihirisha ushirikiano mzuri uliopo kati ya sekta binafsi na wadau wa sekta ya michezo katika kufanikisha ajenda ya Serikali ya kukuza vipaji na kuendeleza michezo nchini.

Naye Meneja wa Ufungaji wa Mgodi wa Barrick Buzwagi, Mhandisi Zonnastraal Mumbi, amesema kutengwa kwa eneo la kujengwa kituo cha michezo katika eneo hilo la mgodi uliofungwa kumezingatia dhamira ya kampuni ya kusaidia jamii sambamba na kuunga mkono jitihada za serikali za kukuza vipaji na kuchochea maendeleo ya michezo nchini.

Top News