Na Janeth Raphael MichuziTv.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dkt. Abdulmajid Nsekela, amesema benki hiyo imejipanga kikamilifu kuhakikisha Watanzania wananufaika na fursa za kiuchumi zitakazotokana na mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027 yatakayofanyika Tanzania, Kenya na Uganda.
Akizungumza katika Bunge Grand Bonanza lililofanyika jijini Dodoma, Dkt. Nsekela amesema CRDB itaendelea kutoa mitaji na huduma mbalimbali za kifedha zitakazowawezesha wananchi, wafanyabiashara na wawekezaji kutumia kikamilifu fursa zitakazotokana na mashindano hayo.
Amesema AFCON si tukio la michezo pekee bali ni jukwaa muhimu la kiuchumi litakalovutia wageni wengi kutoka ndani na nje ya Afrika, hivyo kuongeza mahitaji ya huduma mbalimbali zikiwemo malazi, usafiri, chakula na biashara nyingine ndogondogo na za kati.
"AFCON ina fursa nyingi za kiuchumi. Huu si wakati wa kusherehekea michezo pekee, bali ni fursa ya kukuza biashara, kuongeza ajira na kuinua uchumi wa wananchi. CRDB imejipanga kuhakikisha Watanzania wanapata mitaji na huduma zitakazowawezesha kunufaika na fursa hizo," alisema Dkt. Nsekela.
Aidha, aliipongeza Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa ya kutunga sheria zinazochochea maendeleo ya Taifa na kuimarisha mazingira ya uwekezaji na biashara nchini.
Pia alimpongeza Waziri wa Fedha kwa kuwasilisha bajeti ya Serikali ambayo alisema itaendelea kuboresha maisha ya Watanzania na kuchochea ukuaji wa uchumi, huku akimpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa maono yake ya maendeleo yanayoendelea kufungua fursa mbalimbali za kiuchumi nchini.
Dkt. Nsekela amesema uwepo wa mabalozi wa nchi mbalimbali katika bonanza hilo ni ishara ya mahusiano mazuri ya kidiplomasia na kibiashara ambayo Tanzania imeendelea kujenga na kuyaimarisha kwa miaka mingi.
Amesema michezo ni chombo muhimu cha kuimarisha mshikamano, urafiki na ushirikiano miongoni mwa watu wa mataifa tofauti, huku akisisitiza kuwa ushiriki wa wadau mbalimbali katika bonanza hilo unaonesha namna michezo inavyoweza kuunganisha jamii.
Mkurugenzi huyo amebainisha kuwa CRDB imekuwa mshirika wa maendeleo kwa zaidi ya miongo mitatu na imeendelea kuwa zaidi ya benki kwa kusaidia ukuaji wa biashara, uwekezaji na ajira nchini.
Amengeza kuwa benki hiyo itaendelea kushirikiana na Serikali pamoja na Bunge katika kuhakikisha Tanzania inanufaika kikamilifu na fursa za kiuchumi zinazotokana na matukio makubwa ya kimataifa.
Katika hatua nyingine, Dkt. Nsekela ametoa shukrani kwa uongozi wa Bunge kwa kuendelea kuiamini CRDB na kuipa nafasi ya kuwa mdau mkuu wa Bunge Bonanza, akiahidi kuwa benki hiyo itaendelea kuunga mkono jitihada za maendeleo ya Taifa kupitia sekta za michezo, biashara na uchumi.
Bunge Grand Bonanza lilihusisha ushiriki wa wabunge, watumishi wa Bunge, taasisi mbalimbali za umma na binafsi pamoja na mabalozi wa nchi rafiki, ambapo washiriki walishiriki michezo mbalimbali kwa lengo la kuimarisha afya, mshikamano na ushirikiano.














.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)





















.jpeg)

.jpeg)





