Na Leandra Gabriel, Michuzi TV

MSIMU wa mbio za Mac D Promotions ‘ Mac D Marathon’ kwa mwaka 2026 unatarajiwa kufanyika Julai 4 mwaka huu katika viwanja vya Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC,)  Kwa kauli mbiu ya ‘Go Green With Gas’ yenye kulenga kuhamasisha matumizi ya nishati safi na kutunza misitu.

Akizungumza katika uzinduzi wa mbio hizo uliofanyika katika Hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam Mkurugenzi wa Mipango na Biashara wa Mac D Promotions Denzel Rweyunga amesema kuwa mbio hizo ambazo usajili wake umeanza rasmi leo zinatarajiwa kushirikisha wakimbiaji wa Kilomita 5, 10 na 21 pamoja na mbio za watoto za Kilomita 2.

Amesema kuwa licha ya kuhamasisha utunzaji wa afya kwa kukimbia mbio hizo pia zimelenga kuunga mkono juhudi za Serikali katika kutunza mazingira kwa kuhamasisha matumizi ya nishati safi.

“Tunategemea kuwa na washiriki 3500 katika mbio hizi na maandalizi yameanza mapema ili kuzipa hadhi na viwango vya juu, na tayari usajili umefunguliwa kupitia www.macdmarathon.com na baada ya kujisajili na kufanya malipo kupitia simu au benki washiriki wataweza kupata vifaa zikiwemo tisheti katika vituo mbalimbali vilivyoainishwa.” Amesema.

Akifafanua kuhusu huduma muhimu katika mbio hizo amesema; wamejipanga kwa kuwa na huduma ya kwanza, vituo vya maji safi na salama ya kunywa ya Kilimanjaro, matunda pamoja na ulinzi na washiriki wote watakaofanikiwa kumaliza mbio hizo  watapatiwa medali.

“Mac D Marathon 2026 itarushwa mbashara siku hiyo kupitia vituo vya ITV pamoja na East Africa Televison na baada ya mbio kutakuwa na burudani katika FM Academia chini ya Patcho Mwamba, michezo ya watoto, chakula na vinywaji pamoja na mpira wa miguu kati ya IPP na Mac D promotions.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Riadha Mkoa wa Dar es Salaam Amani Ngoka amesema kupitia mbio hizo ambazo zimelenga kuhamasisha matumizi ya nishati safi, shirikisho litatumia fursa hiyo kusaka vipaji na wawakilishi wa kimataifa katika riadha.

Aidha amewasisitiza wazazi kushiriki mbio hizo na watoto ambao watakimbia Kilomita 2 ili waweze kutambua na kuendeleza vipaji vyao na kuwataka Mac D promotions kufanya mbio hizo kuwa za kimataifa kwa mwaka ujao.

Kwa taarifa zaidi za ushiriki wa mbio hizo pamoja na udhamini Mac D Promotions itapokea kupitia tovuti pamoja na mawasiliano ya simu 0791799848/0702562009 pamoja na barua pepe macdmarathon@gmail.com.

Mbio za Mac D kwa mwaka 2026 zimedhaminiwa na Shirika la Nyumba la Taifa ( NHC ) , Kilimanjaro Natural Mineral Water, Azania Bank, ITV, Eb Maritime Group, Mart Group Ltd kupitia vinywaji vyake pendwa Tanzanite RoyalGin na Tanzanite Crafted For Royalt, Kaluba, Radio One, EATV, Montage na Ayo Tv.

Mkurugenzi wa Mipango na Biashara wa Mac D Promotions Denzel Rweyunga akizungumza wakati wa uzinduzi wa Mac D Marathon mwaka 2026 na kusema kuwa mbio hizo ambazo usajili wake umeanza rasmi leo zinatarajiwa kushirikisha wakimbiaji wa Kilomita 5, 10 na 21 pamoja na mbio za watoto za Kilomita 2. Leo jijini Dar es Salaam.

Mwenyekiti wa Chama cha Riadha Mkoa wa Dar es Salaam Amani Ngoka akizungumza wakati wa hafla hiyo na kueleza kuwa kupitia mbio hizo ambazo zimelenga kuhamasisha matumizi ya nishati safi, shirikisho litatumia fursa hiyo kusaka vipaji na wawakilishi wa kimataifa katika riadha. Leo jijini Dar es Salaam.


NA EMMANUEL MBATILO, MICHUZI TV

Serikali imeeleza dhamira yake ya kuendelea kuimarisha sekta ya fedha nchini ili iwe chachu ya maendeleo ya haraka ya kiuchumi, huku ikisisitiza upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wananchi wote kwa urahisi na gharama nafuu.

Kauli hiyo ilitolewa leo Aprili 9, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa ufunguzi wa jukwaa la wadau wa sekta ya fedha la mwaka 2026, lenye kauli mbiu isemayo “Sekta ya fedha bunifu na yenye uwajibikaji kwa maendeleo endelevu na jumuishi ya jamii na uchumi.”

Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Fedha, Khamis Mussa Omari, aliwataka wadau wa sekta hiyo kutumia jukwaa hilo kutoa mapendekezo yatakayosaidia kuboresha sera, sheria na mifumo ya kifedha, ili kufikia lengo la kuwa na uchumi imara unaotegemea sekta ya fedha ifikapo mwaka 2050.

“Sekta ya fedha ni mhimili muhimu wa maendeleo ya taifa. Tunahitaji kuhakikisha huduma za kifedha zinawafikia wananchi wote kwa urahisi na kwa gharama nafuu,” alisema Waziri Omari.

Ameeleza kuwa jukwaa hilo lina lengo la kuwakutanisha wadau mbalimbali ili kujadili utekelezaji wa Mpango Mkuu wa Maendeleo ya Sekta ya Fedha wa miaka kumi (2021–2029), huku akibainisha kuwa sekta hiyo ina mchango mkubwa katika kukuza uchumi na kuongeza upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wananchi.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu Mwamba, amesema kuwa katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, kumekuwa na mafanikio makubwa katika sekta hiyo, ikiwemo kuongezeka kwa upatikanaji wa huduma za fedha, ongezeko la matawi na mawakala wa benki pamoja na ukuaji wa huduma za fedha kidijitali.

Amebainisha kuwa asilimia 76 ya Watanzania sasa wanapata huduma rasmi za kifedha, hatua inayochangiwa kwa kiasi kikubwa na matumizi ya simu za mkononi na huduma za fedha mtandao.

Naye Naibu Waziri wa Fedha, Mhandisi Mshamu Munde, amesisitiza umuhimu wa kudhibiti hatari za kifedha ikiwemo biashara haramu na matumizi mabaya ya mifumo ya fedha, huku akihimiza usimamizi madhubuti wa teknolojia mpya za kifedha.

Washiriki wa jukwaa hilo walipata fursa ya kujadili changamoto na fursa zilizopo katika sekta ya fedha, hususan katika maeneo ya ubunifu wa teknolojia, ujumuishwaji wa kifedha na uwekezaji.

Jukwaa hilo linatarajiwa kutoa maazimio yatakayosaidia kuimarisha sekta ya fedha na kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.

Wadau waliohudhuria ni pamoja na wawakilishi wa mabenki, taasisi za bima, vyama vya ushirika pamoja na sekta binafsi.






 



Na Oscar Assenga, TANGA

Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Tanga kimetoa maelekezo kwa Halmashauri ya Jiji la Tanga kuhakikisha maeneo ya kukusanyia taka katika soko la Mgandini yanaboreshwa kwa kujazwa kifusi ikiwemo kurekebisha barabara za ndani ili kuimarisha usafi.

Agizo hilo lilitolewa na Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Tanga Rajab Abdurhaman wakati wa ziara yake ambapo alisisitiza umuhimu wa kuhakikisha maji ya mvua yanaelekezwa ipasavyo kwenye mifereji ili kuepusha mafuriko na uharibifu wa miundombinu.

Ziara hiyo ilikuwa ni kufuatilia utekelezaji wa maagizo aliyoyatoa awali kuhusu kuboresha usafi wa soko hilo ambapo viongozi wa Jiji hilo walianza kuyafanyia kazi ikiwemo kuondosha uchafuzi uliokuwepo awali.

Awali, wakati wa ziara yake ya kukagua hali ya usafi, Mwenyekiti huyo hakuridhishwa na mazingira ya soko hilo na kutoa muda wa mwezi mmoja kwa uongozi wa Jiji kuhakikisha hali ya usafi inaboreshwa.

Akizungumza baada ya kufanya ziara ya ufuatiliaji, Rajab aliwapongeza Mstahiki Meya pamoja na viongozi wa Jiji kwa kuchukua hatua na kuanza kutekeleza maelekezo hayo ya CCM.

“Hatuhitaji viongozi wa kulalamika, tunahitaji viongozi wanaochukua hatua kutatua changamoto za wananchi. Mlichokifanya ni kutimiza wajibu wenu,” alisema.

Alisema kuwa hali ya uchafu iliyokuwepo awali haikuwafurahisha viongozi wala wafanyabiashara, hivyo hatua zilizochukuliwa zinaonesha uwajibikaji wa uongozi.

Hata hivyo Mwenyekiti Rajab alisisitiza kuwa atarejea kukagua maendeleo hayo baada ya wiki mbili na kuonya kuwa hataki kusikia visingizio badala ya utekelezaji.

“Ndani ya mwezi mmoja kuanzia Aprili 9 hadi Mei 9, tunatarajia kuona kazi imeanza. Hatutaki hadithi, tunataka vitendo,” alisisitiza.

Aidha, alieleza kuwa Jiji la Tanga ni taswira ya mkoa huo, hivyo linapaswa kuwa safi na lenye mpangilio mzuri.

Alikumbusha kuwa zamani Tanga ilikuwa mji unaojulikana kwa usafi na ustaarabu, hivyo ipo haja ya kurejesha hali hiyo.

Kuhusu huduma za vyoo katika soko hilo, Mwenyekiti alieleza kutoridhishwa na hali iliyopo, akibainisha kuwa choo kilichopo hakitoshelezi mahitaji kutokana na idadi kubwa ya watumiaji.

Alisema kuwa hali hiyo inasababisha baadhi ya watu kulazimika kujisaidia katika maeneo yasiyofaa, jambo linalohatarisha afya za wananchi na wafanyabiashara.

Alisisitiza umuhimu wa Jiji kutafuta suluhisho la kudumu, ikiwemo kuboresha mfumo wa maji taka ili kuendana na ongezeko la watumiaji.

Hata hivyo, aliwapongeza viongozi kwa kuanza mpango wa kujenga choo kipya chenye matundu 12 kitakachosaidia kupunguza changamoto hiyo, hasa katika kipindi hiki ambacho soko linatarajiwa kujengwa upya.

Pia alizungumzia changamoto ya msongamano wa magari yanayoleta bidhaa sokoni hapo, akielekeza kuwepo kwa utaratibu maalum wa magari kuingia na kushusha mizigo kwa mpangilio ili kupunguza msongamano na kuboresha usafi.

Alipendekeza magari yapaki katika maeneo maalum yaliyo nje ya soko, kisha yaingie kwa zamu kushusha bidhaa.

Katika hatua nyengine alisisitiza umuhimu wa kujenga mifereji ya maji ili kuzuia maji ya mvua kutuama au kuingia sokoni, hali inayochangia uchafu na uharibifu wa mazingira.

Alimalizia kwa kuwataka viongozi wa Jiji kuwa karibu na wananchi na kushughulikia changamoto zao kwa vitendo, akibainisha kuwa wananchi hao ndio chanzo cha mapato ya Jiji kupitia kodi.

Kwa upande wake, Naibu Meya Khalid Rashid alisema kuwa Jiji lina mpango wa kuboresha miundombinu ya ndani ya soko, ikiwemo njia za kupita ili kuondoa changamoto ya matope wakati wa mvua. Alibainisha kuwa kazi hiyo inatarajiwa kuanza ndani ya wiki moja.

Mwisho.

MAMLAKA ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) imewatangazia waingizaji wa mizigo mikubwa ya forodha ya bidhaa za Dawa, Vifaa Tiba na Vitendanishi nchini, kuwa mifumo ya TANCIS-TRA na RIMS-TMDA imeunganishwa ili kuongeza ufanisi katika kuingiza na kutoa shehena za bidhaa hizo nchini kwa njia ya kielektroniki.  

Kwa mujibu wa taarifa kwa Umma iliyotolewa na Mkurugenzi Mkuu wa TMDA, Dk. Adam Fimbo ameeleza kuwa, Lengo kuu la muunganiko huo ni kurahisisha michakato ya uombaji vibali kuwa na sehemu moja ya kuingiza taarifa, pamoja na kuboresha ufuatiliaji na shughuli za udhibiti wa maombi ya kuingiza na kutoa bidhaa nchini.

"Mnajulishwa rasmi kuwa kuanzia tarehe 1 Mei, 2026 maombi yote yaliyokuwa yanapitia TMDA-RIMS na TRA-Forodha kwa ajili ya kutolea taarifa (declaration) yatafanyika moja kwa moja katika mfumo wa TANCIS.  

Ili kuepusha Hoja zisizo za lazima na kurahisisha huduma za upatikanaji wa vibali, mnakumbushwa kuzingatia; Usahihi wa taarifa za bidhaa zinazosimamiwa na TMDA (ikijuimuisha namba za usajili za bidhaa na majengo); na Wadau wote watatakiwa kushirikiana na Wakala wa Forodha kwa ukaribu ili kuthibitisha usahihi wa taarifa za kitaalam na nyaraka hitajika." Imeeleza taarifa hiyo kwa Umma.

Aidha, TMDA imewataka kuzingatia kuwa, tangazo hilo  linawahusu waingizaji wa mizigo mikubwa ya forodha, na si waingizaji kwa matumizi binafsi (personal use).

Na Mwandishi wetu, Dodoma

 Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imesema ujenzi wa moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST utachangia kuongeza uwajibikaji, uwazi na ufanisi kwenye mnyororo wa ugavi.

Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando amebainisha hayo wakati wa uzinduzi rasmi wa Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025 na kuongeza kuwa Moduli hiyo imewaunganisha wazabuni wote na Taasisi nunuzi nchini ili kuongeza uwajibikaji katika utatuzi wa migogoro inayotokana na michakato ya ununuzi wa umma. 

“PPAA ni moja kati ya taasisi zinazosimamia ununuzi wa umma nchini, matumizi ya moduli hiyo katika mnyororo wa ugavi yatachangia kutoa maamuzi kwa haki na wakati na kuwezesha miradi ya Serikali kutekelezwa kwa wakati uliokusudiwa,” amesema Bw. Sando.

Pamoja na mambo mengine, Bw. Sando amebainisha kuwa matumizi ya Moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika ununuzi wa umma yatasaidia kuongeza uwazi, kupunguza gharama, kuokoa muda, utunzaji wa nyaraka na hivyo kuongeza ufanisi katika hukumu zinazotolewa kutokana na michakato mbalimbali ya zabuni za umma.

Bw. Sando ameongeza kuwa, PPAA imefanikiwa kushiriki katika utungwaji wa Sera ya Taifa ya Mnyororo wa Ugavi, Sheria ya Ununuzi wa Umma, Kanunuzi za Ununuzi wa Umma na Kanuni za Rufaa za Ununuzi wa Umma ambapo yote ni michango wa Mamlaka ya Rufani katika mnyororo wa ugavi.

Kadhalika, Mamlaka ya Rufani inatarajia kuboresha kipengele cha makundi maalum na vijana ambapo inategemea kuboresha gharama au tozo za kesi kwa makundi maalum pamoja na kuelekeza nguvu kwa vijana na kuhakikisha wanapata fursa ya kudai haki zao katika michakato ya ununuzi wa umma.

Awali akizindua Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba (Mb), amezielekeza mamlaka, taasisi na wadau wote wanaosimamia utekelezaji wa Sera hiyo kuhakikisha wanatekeleza majukumu yao kwa kuzingatia misingi ya utawala bora, uwazi na utawala wa sheria.‎

‎Waziri Mkuu ametoa maelekezo hayo wakati akizundua Sera hiyo kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan. Dkt. Nchemba amesema changamoto zinazoikumba sekta ya ununuzi wa umma hazitokani na sera au sheria zilizopo, bali ni uzembe na mitazamo ya baadhi ya watendaji.‎

‎Ameongeza kuwa taarifa za ukaguzi kutoka kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) pamoja na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) zinaonesha wazi kuwa kasoro nyingi zinasababishwa na utekelezaji dhaifu wa sheria, kanuni na taratibu zilizopo.

“Sehemu kubwa ya changamoto hizo zinatokana na hulka, tabia na mitazamo ya watendaji. Hivyo, ni lazima tubadilike ili kufikia malengo ya sera hii,” amesisitiza Dkt. Mwigulu.

Aidha, Waziri Mkuu, amezitaka wizara, taasisi na mamlaka zote kufanya mapitio ya sera, sheria na kanuni zinazokinzana na sera hiyo ili kuweka mazingira rafiki ya utekelezaji wake.

Naye Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar amesema sera hiyo ni mwongozo muhimu utakaosaidia kuimarisha mifumo ya ugavi katika sekta ya umma, kuongeza uwajibikaji katika matumizi ya fedha za umma na kudhibiti vitendo vya rushwa.‎
Balozi Khamis ameongeza kuwa utekelezaji wa sera hiyo utaongeza ajira, kuimarisha mnyororo wa thamani na kuchochea mageuzi makubwa ya kiuchumi kuelekea dira ya maendeleo ya mwaka 2050.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba (Mb), akizungumza na viongozi wa Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA), wakati alipotembelea banda ya maonesho katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma, kabla ya kuzindua rasmi Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025.Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba (Mb), (Katikati Kulia), akiwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), na viongozi wengine wakisikiliza maelezo kutoka kwa Katibu Mtendaji wa Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA), Bw. James Sando (kushoto), kuhusu mchango wa PPAA katika Mnyororo wa Ugavi, wakati Mhe. Waziri Mkuu alipotembelea banda ya maonesho katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma, kabla ya kuzindua rasmi Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025.Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba (Mb), akizindua rasmi Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025 katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma.
Sehemu ya viongozi mbalimbali walioshiriki katika uzinduzi wa Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025 katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma.




 

MSIMU wa mbio za Mac D Promotions ‘ Mac D Marathon’ kwa mwaka 2026 unatarajiwa kufanyika Julai 4 mwaka huu katika viwanja vya Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC,)  Kwa kauli mbiu ya ‘Go Green With Gas’ yenye kulenga kuhamasisha matumizi ya nishati safi na kutunza misitu.

Akizungumza katika uzinduzi wa mbio hizo uliofanyika katika Hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam Mkurugenzi wa Mipango na Biashara wa Mac D Promotions Denzel Rweyunga amesema kuwa mbio hizo ambazo usajili wake umeanza rasmi leo zinatarajiwa kushirikisha wakimbiaji wa Kilomita 5, 10 na 21 pamoja na mbio za watoto za Kilomita 2.

Amesema kuwa licha ya kuhamasisha utunzaji wa afya kwa kukimbia mbio hizo pia zimelenga kuunga mkono juhudi za Serikali katika kutunza mazingira kwa kuhamasisha matumizi ya nishati safi.

“Tunategemea kuwa na washiriki 3500 katika mbio hizi na maandalizi yameanza mapema ili kuzipa hadhi na viwango vya juu, na tayari usajili umefunguliwa kupitia www.macdmarathon.com na baada ya kujisajili na kufanya malipo kupitia simu au benki washiriki wataweza kupata vifaa zikiwemo tisheti katika vituo mbalimbali vilivyoainishwa.” Amesema.

Kwa undani wa taarifa hii tembelea www.michuzi.co.tz




 


Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda Maalum imefanya kikao kazi na wadau wa habari, wakiwemo wamiliki, wahariri na waandishi wa habari, kwa lengo la kujenga ushirikiano endelevu kati ya taasisi hiyo na vyombo vya habari nchini.


Kikao kazi hicho kimefanyika Aprili 9, 2026 katika ukumbi wa mikutano wa Shule ya Uongozi Mwalimu Nyerere, Kibaha, mkoani Pwani.

Akifungua kikao hicho, Katibu Msaidizi wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda Maalum, Bi. Elizabeth Komba, amesema vyombo vya habari si kioo tu cha jamii bali pia ni nyenzo muhimu ya kuunda na kukuza maadili nchini.

“Tunaamini kuwa vyombo vya habari vina nafasi ya kipekee katika kukuza maadili, uwajibikaji na uwazi katika jamii. Kwa maneno mengine, nyinyi ni nguzo muhimu katika kujenga au kubomoa maadili katika jamii. Hivyo, tutumie tasnia hii kujenga jamii yenye uadilifu,” amesema Bi. Komba.

Aidha, ameongeza kuwa vyombo vya habari vina nafasi kubwa katika kukuza uwajibikaji kwa kufichua vitendo vya rushwa, ubadhilifu na matumizi mabaya ya madaraka, kwa kuweka wazi ukweli unaowezesha wahusika kuwajibika.

“Kama tukitumia vyombo vya habari kwa njia sahihi, tunaweza kujenga jamii yenye uadilifu, uwazi na haki. Lakini tukivitumia vibaya, tunaweza kuharibu maadili, kuleta migawanyiko miongoni mwetu na hatimaye kujenga jamii isiyo na uzalendo,” alisisitiza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Mipango, Ufuatiliaji na Tathmini kutoka Sekretarieti hiyo, Bw. Omary Juma, amesema ushirikiano huo utakuwa endelevu, huku wakiahidi kuendelea kukutana mara kwa mara ili kujadili mbinu bora za kukuza na kuimarisha maadili nchini.

Katibu Msaidizi Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda Maalum Bi. Elizabeth Komba akizungmza wakati akifungua Kikao Kazi cha wamiliki, wahariri na waandishi wa habari wa Kanda hiyo. Kikao hicho kimefanyika katika ukumbi wa mikutano wa Shule ya Uongozi Mwalimu Nyerere mjini Kibaha mkoani Pwani tarehe 09 Aprili, 2026.





 


▪️Asema Serikali itaimarisha vitengo vya tathmini na ufuatiliaji kila wizara

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuboresha bajeti ya elimu wakati ikitekeleza mtaala mpya wa elimu ili kuziba mianya ya mahitaji shuleni.

“Kwa kuwa tunaenda katika mtaala mpya wa elimu, tutaendelea kuboresha bajeti. Tutaendelea kuboresha bajeti kwa sababu mahitaji yanaongezeka kila wakati katika kumfanya mtoto asome vizuri,” amesema.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo Bungeni jijini Dodoma, leo (Alhamisi, Aprili 9, 2026) wakati akijibu swali la Mbunge wa Segerea, Agnesta Lambert Kaiza, kwenye kipindi cha maswali ya papo kwa papo kwa Waziri Mkuu ambaye alitaka kujua kauli ya Serikali juu ya kukomesha michango holela inayotozwa shuleni.

Dkt. Mwigulu amesema Serikali haina shida na michango ya chakula ambayo imekuwa ikitolewa shuleni lakini akasisitiza kuwa endapo kutatokea michango mingine yoyote, ni lazima ifuate miongozo ya serikali na ipate baraka za Wakuu wa Mikoa husika.

Akitoa mfano wa michango ambayo haikubaliki, Waziri Mkuu amesema akiwa ziarani mkoani Katavi, alipokea malalamiko ya Mama mmoja ambaye mwanaye alizuiwa kujiunga na shule ya sekondari hadi atoe sh. 50,000/- ya dawati.

“Nilielekeza yule mtoto arudishwe shuleni na nimpongeze Mkuu wa Mkoa ambaye amenijulisha kuwa yule mtoto amesharudi shuleni. Lakini pia nilielekeza yule mwalimu mkuu naye aitwe na mamlaka za nidhamu, ahojiwe kwa uzembe wa kuona mtoto anakosa masomo kwa miezi miwili na wao wakaendelea na maisha kana kwamba hakuna jambo lililotokea,” amesema.

Mbali na changamoto hiyo, Waziri Mkuu amewapongeza walimu nchini kwa kujitoa bila kuchoka ili kuhakikisha watoto wa Kitanzania wanapata elimu bora. “Sote tunatambua kuwa walimu wengi wamejitoa sana katika baadhi ya maeneo. Licha ya wingi watoto na uchache wa walimu, kwa juhudi zao wamehakikisha wanakamilisha syllabus zao ili watoto wetu wapate elimu bora.”

Akielezea kuhusu uwepo wa walimu wa kujitolea katika baadhi ya shule, Waziri Mkuu amesema alishatoa maelekezo kwamba malipo ya walimu wa aina hiyo yatoke kwenye mapato ya ndani ya Halmashauri husika badala ya kuwataka wazazi wachangie malipo yao.

“Wazo la kuwa na walimu wa kujitolea ni jema, na sisi wakati tunasoma tulipata mafunzo ya ziada (tuition) kwa walimu wa aina hii. Wazo la kuwa na walimu wanaojitolea ni jema lakini malipo yao yasilipwe na wazazi, badala ya kwenda kwenye michango, Mamlaka za Serikali za Mitaa watumie mapato ya ndani.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kuimarisha vitengo vya tathmini na ufuatiliaji katika kila wizara ili viweze kufanya kazi kwa ufanisi zaidi. “Kwenye kila wizara, kuna hivi vitengo vya ufuatiliaji na tathmini. Tunapanga kuongeza bajeti zao ili viweze kutimiza wajibu wao katika ufuatiliaji wa miradi na shughuli zote za Serikali.

Alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Monduli, Isack Joseph Copriano aliyetaka kujua  Serikali ina mkakati gani wa kuimarisha timu ya tathmini na ufuatiliaji ili kuharakisha majibu ya wananchi na hususan kero zao. 

Alisema katika kuimarisha mawasiliano na wananchi, Serikali imeanzisha kituo cha kupokea simu (Call Centre) yenye namba 190 ambapo mwananchi mwenye shida yoyote anaweza kupiga simu na kutoa kero yake na kwamba atajulishwa majibu yake kupitia kituo hicho.

Amesema Serikali inataka kurejesha utaratibu wa kila kiongozi kubeba hoja za wananchi kupitia rejesta ambazo zitakuwa zinatumika kwenye ofisi za viongozi kurekodi kero za wananchi na kutoa mrejesho serikalini kila mwisho wa mwezi.

“Utaratibu wa kupokea kero siyo wa kwenye ziara tu, kila mwezi viongozi watapaswa kutoa taarifa ya idadi ya wananchi waliowahudumia na majibu waliyowapa wakionesha hoja zipi walipokea, namba za simu za wananchi waliohudumiwa na hizo hoja zimetatuliwa vipi.” 

“Tunataka kurejesha utaratibu wa kila kiongozi kubeba hoja za wananchi na siyo kuacha wananchi waende kutafuta majibu kwa viongozi,” alisisitiza.



Na: OWM (KAM) - Dodoma

Serikali imeendelea kuhakikisha miradi mikubwa inayotekelezwa ama inayoanzishwa inatoa fursa za Ajira kwa Watanzania zaidi.

Aidha, utekelezaji wa suala hilo linatekelezwa kupitia utekelezaji wa Sera na Sheria ambapo miongoni mwa Sera na Sheria hizo ni pamoja na Sera ya Taifa ya Ajira ya mwaka 2008, Sera ya Taifa ya Nishati ya mwaka 2015, Sheria ya Mafuta, Sura 392 pamoja na Sheria ya Madini Sura 123.

Hayo yamebainishwa Aprili 9, 2026 Bungeni Jijini Dodoma na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Rahma Kisuo wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum Mhe. Jasmine Chesco, lililouliza Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha vijana wanapata ajira katika miradi mikubwa kama SGR na viwanja vya ndege.

 Akijibu swali hilo, Mhe. Rahma amesema Kupitia miradi mikubwa inayotekelezwa nchini, vijana wananufaika na fursa za ajira ambapo zaidi ya ajira 35,000 zimetolewa katika ujenzi wa Reli ya SGR, zaidi ya ajira 10,000 katika mradi wa ujenzi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP), na zaidi ya ajira 2,497 zimetolewa katika ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Msalato Dodoma sambamba na upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere. 

Vilevile, amesema zaidi ya ajira 1,500 zimetolewa katika ujenzi wa daraja la Kigongo – Busisi, na zaidi ya ajira 3,000 katika upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam.

Katika hatua nyingine, Mhe. Rahma amesema Serikali inahakikisha vijana wanapata ujuzi unaohitajika katika miradi hiyo kupitia Programu ya Taifa ya Kukuza Ujuzi inayowawezesha vijana kupata ajira na kushiriki kwa ufanisi katika kazi za viwandani na miradi mikubwa ya kimkakati.

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Rahma Kisuo 

Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro Bw. Abdul-Razaq Badru leo tarehe 9 Aprili, 2026 amepuliza rasmi Kipenga cha shindano la mwezi mmoja la Safari Field Challenge akisisitiza kwamba Ngorongoro ni nyumbani kwa kila binadamu kutokana na chimbuko la historia linalobainishwa kisayansi.

Akizindua shindano hilo Kamishna Badru amewashukuru washiriki nane (8) wa shindano hilo kwa kuitika wito wa Ngorongoro na kuwaeleza kuwa Hifadhi ya Ngorongoro ni zaidi ya Kreta hasa kutokana na kuwa na utamaduni, asili, chimbuko la binadamu wa kale, siri ya Binadamu na maisha yake, Nyayo za Laetoli zenye umri za zaidi ya miaka milioni 3.6, mchanga unaohama, kushuhudia pumzi ya kwanza ya Nyumbu eneo la Ndutu, kuona Wanyama wakubwa watano katika eneo moja, mlima Lolmalasian ambao wa tatu kwa urefu Tanzania, misitu, mimea na ndege mbalimbali.

“Karibuni Ngorongoro ambapo ni nyumbani kwa sisi sote, mtapata uzoefu ya maajabu mbalimbali, kuyahisi, kuyaishi, kufurahia, kuyahadithia na kuwasaidia kupata ujuzi ambao utawafanya muwe mabalozi wazuri kuwaelezea watu wengine mkusanyiko wa maajabu yaliyoko Ngorongoro” Alisema Kamishna Badu.

Kamishna Badru amewapa changamoto washiriki wa shindano hilo kuwa watundu wa kuifahamu Ngorongoro, kuisemea Ngorongoro kwa mtazamo mpya wa sauti moja ambapo kwa kushirikiana na Azam Media hadithi, historia, maajabu ya Ngorongoro itasimuliwa na kufika pembe nne za dunia kuwa Ngorongoro sio kivutio cha utalii pakee bali ni Nyumbani kwa kila Binadamu ambapo historia yao ilianza.

Kamishna Msaidizi Mwandamizi anayesimamia Huduma za Utalii na masoko Mariam Chuma Kobelo amewaeleza washiriki wa Safari Field Challenge kuwa Tanzania ina vitu vingi vya Kujivunia,lakini Ngorongoro kuna vingi zaidi na kuwasisitiza washiriki wa shindano hilo kwenda kujifunza, kuifahamu na kuisimulia Ngorongoro kuwa ni zaidi ya Kasoko ya Ngorongoro.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Tanzania Tour Guide Fondation (TTGF) Mosses Njole ameleza kuwa washiriki wote 8 wako timamu na wamejiandaa kikamilifu kushiriki shindano hilo na kuwapongeza Ngorongoro kwa kuwa wadhamini wakuu na wadau wengine wakiwepo Azam Media ambayo imekuwa sehemu ya kusimulia maajabu ya Ngorongoro.












KAMPUNI ya Miracle Concierge imetangaza kufungua kituo kipya cha abiria chenye huduma maalum kiitwacho Uhuru Terminal & Lounge katika uwanja wa Kimataifa wa Kilimanjaro kuanzia Julai 1, 2026, hatua inayolenga kuboresha uzoefu wa safari kwa wageni wanaotumia ukanda wa utalii wa kaskazini mwa Tanzania.

Kituo hicho kinatajwa kuwa miongoni mwa vituo vya kwanza vya binafsi katika kanda ya Kaskazini mwa Tanzania, kikilenga kuwapatia wasafiri huduma ya faragha na urahisi zaidi tofauti na vituo vikuu ya abiria.

Kwa mujibu wa kampuni hiyo, kituo hicho kitatoa huduma maalum zikiwemo usajili wa safari (check-in), msaada wa huduma za uhamiaji pamoja na taratibu za kupanda ndege, hali itakayowezesha wageni kuepuka msongamano wa abiria katika kituo kikuu.

Mradi huo hivi karibuni ulitembelewa na kufanyiwa ukaguzi na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya ndege Tanzania (TAA), Abdul Mombokaleo, pamoja na Mkurugenzi wa Kiwanja cha ndege cha Kilimanjaro, Injinia Rehema Myeya, wakiongozana na viongozi wengine wa uwanja huo wakati ujenzi ukiendelea.

Uwanja wa Kimataifa wa Kilimanjaro ni lango muhimu kwa watalii wanaotembelea vivutio vikuu vya utalii kaskazini mwa Tanzania ikiwemo Mbuga ya wanyama ya Serengeti, Hifadhi Ngorongoro na Mlima Kilimanjaro. Miracle Concierge imesema ujenzi wa Kituo hiyo unalenga kurahisisha safari kwa kupunguza ucheleweshaji na kuongeza faraja kwa abiria wanaowasili na wanaoondoka.

Kituo hicho kitakuwa na muundo wa ghorofa mbili uliobuniwa kwa kuzingatia mandhari ya utamaduni wa Tanzania. Ndani yake kutakuwa na maeneo ya mapumziko yenye vinywaji, vyumba vya kuoga na sehemu tulivu za kukaa.

Pia kutakuwepo vyumba binafsi vya kupumzikia, vyumba vya mikutano na maeneo ya uratibu kwa waendeshaji wa utalii na washirika wa safari.

Akizungumza Aprili 8, 2026, Mwanzilishi na Mtendaji Mkuu wa Miracle Collection, Hasnain Sajan, alisema mradi huo ni sehemu ya mkakati wa kampuni hiyo wa kuboresha safari za wageni wanaotembelea Tanzania.

Alisema lengo lao ni kuondoa changamoto katika safari za wasafiri na kuhakikisha kila hatua ya safari inakuwa rahisi, ya faragha na yenye mpangilio mzuri tangu mgeni anapowasili.

Aidha,Kituo cha Uhuru ni sehemu ya mtandao unaokua wa huduma za ukarimu unaoendeshwa na Miracle Collection nchini, ukiwemo Boma Lounge iliyopo Arusha na Ziwani Lounge iliyopo Ziwa Manyara, huku kituo kingine cha aina hiyo kikitarajiwa kujengwa Dar es Salaam.

Huduma za kituo hicho zitapatikana kupitia vifurushi vinavyohitaji kuweka nafasi mapema, huku idadi ya watumiaji ikidhibitiwa kulingana na muda na nafasi zilizopo.

Kwa mujibu wa kampuni hiyo, vifurushi hivyo vitajumuisha msaada wa huduma za uhamiaji, urahisishaji wa ukaguzi wa usalama, matumizi ya lounge, vinywaji, vyumba vya kuoga, maeneo ya kuchezea watoto pamoja na sehemu tulivu za kupumzika.

Gharama za huduma zitajumuisha kodi ya ongezeko la thamani (VAT), huku watoto walio chini ya miaka miwili wakiruhusiwa kutumia huduma hizo bila malipo.

Miracle Concierge imesema ujenzi wa mradi huo unaendelea vizuri na unatarajiwa kukamilika kwa wakati ili uzinduliwe rasmi Julai 2026.

Top News