Na Benny Mwaipaja, Dar es Salaam

Serikali ya Tanzania imerejea tena dhamira yake ya kushirikiana kwa karibu na Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC) ili kuongeza uwekezaji wa sekta binafsi, kupanua miundombinu na kuharakisha Mpango wa Taifa wa mabadiliko ya nishati chini ya Dira ya Taifa ya Maendeleo (DIRA 2050).

Akizungumza katika kikao na Mkurugenzi wa IFC Kanda ya Afrika Mashariki, Bi. Mary Porter Peschka, Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), alisifu mchango wa muda mrefu wa IFC katika kukuza sekta binafsi nchini Tanzania, akisisitiza kuwa ushirikiano huo utaendelea kuwa muhimu katika kufanikisha malengo ya muda mrefu ya maendeleo ya taifa.

Mhe. Balozi Omar alibainisha mchango mkubwa wa IFC katika kukuza ukuaji wa sekta binafsi kupitia ufadhili wa fedha, ubunifu na programu za kujenga uwezo wa kitaasisi.

Alieleza kuwa utekelezaji wa DIRA 2050, unaokadiriwa kugharimu takribani dola za Marekani trilioni 1, utategemea kwa kiasi kikubwa uwekezaji wa sekta binafsi unaotarajiwa kuchangia zaidi ya asilimia 70 ya gharama za utekelezaji.
“Ushirikiano endelevu na IFC ni muhimu katika kuhamasisha rasilimali, kuchochea ushiriki wa sekta binafsi na kuhakikisha mageuzi ya kijamii na kiuchumi ya Tanzania yanafikiwa,” alisema Mhe. Balozi Omar.

Mhe. Balozi Omar pia alizungumzia mafanikio yaliyopatikana kupitia Mpango wa Taifa wa Nishati (Mission 300 Tanzania Energy Compact), unaolenga kuongeza upatikanaji wa umeme na nishati safi kufikia mwaka 2030.

Kati ya Januari 2025 na Januari 2026, upatikanaji wa umeme nchini umeongezeka kutoka asilimia 78.4 hadi 85.5, uunganishaji wa kaya kufikia gridi umeongezeka kutoka asilimia 46 hadi 52.1, na sehemu ya nishati inayotokana na vyanzo vinavyoweza kurejelewa imepanda kutoka asilimia 61.8 hadi 69.

Hata hivyo, Mhe. Balozi Omar alisisitiza haja ya kuendelea kuvutia uwekezaji zaidi ili kupanua huduma hasa vijijini na kukuza matumizi ya nishati safi kwa kupikia.

Aliitaka IFC kutumia utaalamu wake wa kimataifa kufadhili miradi ya kimkakati ya nishati kama mitambo ya umeme wa maji ya Kikonge, Ruhudji na Rumakali, pamoja na miradi ya jua, upepo na jotoardhi iliyomo ndani ya mpango huo.

Aidha, alieleza jitihada za serikali katika kuvutia mitaji ya sekta binafsi kupitia miradi ya Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPPs) ambapo Kituo cha Ubia Kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPPC) kimeandaa orodha ya kitaifa inayojumuisha miradi 113 iliyoko katika hatua mbalimbali za maandalizi na utekelezaji katika sekta muhimu ikiwemo usafiri, biashara, kazi, na kilimo. Miradi 10 muhimu inatarajiwa kuendelezwa katika mwaka wa fedha 2026/27, ikihitaji msaada wa kifedha kwa ajili ya maandalizi.

Mhe. Balozi Omar aliiomba IFC kutoa ushauri wa kitaalamu na msaada wa kitaasisi ili kusaidia PPPC na taasisi za serikali katika kuandaa miradi kulingana na viwango vya kimataifa.

“Kuimarisha uwezo wa taasisi zetu na kuoanisha miradi ya PPP na viwango bora vya kimataifa kutaimarisha imani ya wawekezaji na kuharakisha utekelezaji,” alisema Balozi Omar.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa IFC Kanda ya Afrika Mashariki, Bi. Mary Porter Peschka, amesema kuwa Taasisi yake ambayo ni miongoni mwa Taasisi zilizochini ya Benki ya Dunia, iko tayari kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kukuza sekta binafsi katika Nyanja mbalimbali za kukuza biashara, nishati, kilimo biashara na uwekezaji ili kuinua maisha ya watu na uchumi wa Tanzania.

Kwa mujibu wa tathmini ya IFC ya mwaka 2025, taasisi hiyo imewekeza takribani dola milioni 197.4 katika nusu ya kwanza ya mwaka wa fedha 2026, kupitia mikopo ya muda mfupi iliyolenga kuchochea shughuli za sekta binafsi.
Kiasi cha uwekezaji wa IFC nchini Tanzania kimefikia dola milioni 315.9, ambapo asilimia 74 imeelekezwa katika sekta ya huduma za kifedha na asilimia 26 katika viwanda, kilimo-biashara, na huduma nyingine.

IFC pia inaunga mkono utekelezaji wa Mradi wa Usafiri wa Mabasi yaendayo Haraka (BRT) jijini Dar es Salaam kupitia huduma za ushauri wa PPP, pamoja na kutekeleza Mpango wa Kitaifa wa Jinsia (Gender Program) wenye thamani ya dola milioni 6.3 hadi mwaka 2028, unaolenga kuongeza ushiriki wa wanawake katika shughuli za kibiashara.

Kikao hicho kilihudhuriwa na maafisa waandamizi kutoka Wizara ya Fedha, Wizara ya Nishati, Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPPC), pamoja na wawakilishi wa IFC.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akiongoza kikao chake na ujumbe kutoka Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC) Kanda ya Afrika Mashariki, ukiongozwa na Mkurugenzi wake, Bi. Mary Porter Peschka, baada ya kukutana na kuzungumza katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, ambapo walijadili masuala mbalimbali ya kushirikiana katika ili kuongeza uwekezaji wa sekta binafsi, kupanua miundombinu na kuharakisha mpango wa taifa wa mabadiliko ya nishati chini ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 (DIRA 2050).

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akizungumza jambo wakati akiongoza kikao na ujumbe kutoka Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC) Kanda ya Afrika Mashariki, ukiongozwa na Mkurugenzi wake, Bi. Mary Porter Peschka, baada ya kukutana na kuzungumza katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, ambapo walijadili masuala mbalimbali ya kushirikiana katika ili kuongeza uwekezaji wa sekta binafsi, kupanua miundombinu na kuharakisha mpango wa taifa wa mabadiliko ya nishati chini ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 (DIRA 2050).

Mkurugenzi wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC) Kanda ya Afrika Mashariki, Bi. Mary Porter Peschka, akizungumza jambo wakati wa alipoongoza ujumbe wa IFC kufanya mazungumzo na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, ambapo walijadili masuala mbalimbali ya kushirikiana katika ili kuongeza uwekezaji wa sekta binafsi, kupanua miundombinu na kuharakisha mpango wa taifa wa mabadiliko ya nishati chini ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 (DIRA 2050).

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (kulia), akiteta jambo na kiongozi wa ujumbe kutoka Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC) ambaye pia ni Mkurugenzi wa Shirika hilo Kanda ya Afrika Mashariki, Bi. Mary Porter Peschka, mara baada ya kikao chao kilichofanyikakatika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, ambapo walijadili masuala mbalimbali ya kushirikiana katika ili kuongeza uwekezaji wa sekta binafsi, kupanua miundombinu na kuharakisha mpango wa taifa wa mabadiliko ya nishati chini ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 (DIRA 2050).


Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akiagana na Mkurugenzi wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC) Kanda ya Afrika Mashariki, Bi. Mary Porter Peschka, baada ya kukutana na kuzungumza katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, kuhusu masuala mbalimbali ya kushirikiana katika ili kuongeza uwekezaji wa sekta binafsi, kupanua miundombinu na kuharakisha mpango wa taifa wa mabadiliko ya nishati chini ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 (DIRA 2050).


Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (Katikati), Mkurugenzi wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC) Kanda ya Afrika Mashariki, Bi. Mary Porter Peschka, na maafisa waandamizi kutoka Wizara ya Fedha, Wizara ya Nishati, Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPPC), pamoja na wawakilishi wa IFC, wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kukutana na kufanya mazungumzo katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, kuhusu masuala mbalimbali ya kushirikiana katika ili kuongeza uwekezaji wa sekta binafsi, kupanua miundombinu na kuharakisha mpango wa taifa wa mabadiliko ya nishati chini ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 (DIRA 2050).

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Dar es Salaam)

Farida Mangube Morogoro

Kampuni ya Coca-Cola imewekeza zaidi ya Shilingi bilioni 5 katika mradi wa kulinda na kurejesha vyanzo vya maji vya Bonde la Wami-Ruvu, hatua inayolenga kunufaisha zaidi ya wakulima 2,000 wanaotegemea rasilimali hiyo kwa maisha na shughuli zao za kiuchumi.

Fedha hizo zimewekezwa kwenye Mradi unaojulikana kama NBS4WATER unatekelezwa na IUCN kwa kushirikiana na Serikali kupitia Bodi ya Maji ya Bonde la Wami-Ruvu, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Coca-Cola katika kuhakikisha upatikanaji wa maji safi, kuhifadhi mazingira, na kusaidia wakulima kutumia mbinu Bora za kilimo zinazostahimili mabadiliko ya tabianchi.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mradi mjini Morogoro, Meneja Mkuu wa Coca-Cola Kwanza, David Chait, amesema uwekezaji huo ni sehemu ya dhamira ya kampuni hiyo kuhakikisha maji yanapatikana kwa shughuli za kiuchumi.

“Bonde la Wami-Ruvu lina mchango mkubwa kwa maisha ya watu na uchumi wa taifa. Kulinda vyanzo vyake ni jukumu letu sote,” alisema Chait.

Kwa Meneja wa mradi kutoka IUCN, Doyi Mazenzele, amesema zaidi ya wakulima 2,000 watanufaika moja kwa moja kwa kufundishwa kilimo kinachokabiliana na mabadiliko ya tabianchi, huku mradi ukitarajiwa kurejesha zaidi ya hekari 3,000 za ardhi na kuongeza upatikanaji wa maji kwa lita milioni 548.

Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mkurugenzi Msaidizi wa Wizara hiyo, Rosemary Rwegubisa, amesema serikali imepiga marufuku shughuli zote za kibinadamu ndani ya mita 60 kutoka vyanzo vya maji, huku hatua mbadala ikiwemo upandaji miti, ufugaji wa nyuki na uchimbaji wa visima, ili wananchi waweze kujipatia kipato bila kuharibu mazingira.

Kaimu Mkurugenzi wa Bonde la Wami-Ruvu, Juvenalis Tarimo, alisisitiza umuhimu wa ushiriki wa wananchi katika kulinda rasilimali hizo, akibainisha kuwa mafanikio ya mradi yataegemea ushirikiano wa karibu na jamii.

Makamu wa Rais wa Coca-Cola Afrika Mashariki na Kati, Alfred Olajide, alisema mradi huo ni sehemu ya jitihada za kimataifa za kampuni hiyo kukabiliana na changamoto ya uhaba wa maji duniani.

Uzinduzi huo uliambatana na zoezi la upandaji miti zaidi ya 2,000 kando ya Bwawa la Mindu mjini Morogoro, ikionyesha kuanza kwa utekelezaji wa hatua za vitendo katika kulinda na kurejesha vyanzo vya maji.





 

WATUMISHI  wa Tume ya Ushindani Ofisi ya Kanda ya Ziwa wametoa elimu kwa wadau mbalimbali, wakiwemo wanafunzi, waandishi wa habari na wafanyabiashara, walipotembelea Banda la Kliniki ya Walaji katika Manispaa ya Musoma Mkoani Mara.

Banda hilo limegeuka kuwa kitovu cha maarifa, likiwavutia wengi waliotaka kuelewa kwa undani haki zao kama walaji pamoja na namna bora ya kushiriki katika soko kwa uadilifu na uelewa mpana.

Akitoa elimu hiyo, Mkuu wa Kanda ya Ziwa FCC, Bw. Mdimi, amesisitiza umuhimu wa walaji kuwa na uelewa wa haki zao ili kujilinda dhidi ya bidhaa duni, huduma zisizo na viwango na vitendo vya udanganyifu vinavyoweza kujitokeza sokoni.

"Amebainisha kuwa elimu kwa walaji ni silaha muhimu katika kujenga uchumi imara unaozingatia haki na usawa kwa wote."amesema Bw.Mdimi

Kwa upande wa wafanyabiashara, wamekumbushwa umuhimu wa kuendesha shughuli zao kwa kuzingatia sheria za ushindani wa haki, wakielezwa kuwa uaminifu kwa wateja ni msingi wa mafanikio ya biashara yoyote endelevu.

Elimu hiyo imewajengea uelewa mpya kuhusu wajibu wao katika kulinda maslahi ya walaji.

Wanafunzi  wameahidi kuwa mabalozi wa elimu hiyo katika jamii zao, huku waandishi wa habari wakiahidi kueneza ujumbe huo kwa umma kupitia vyombo vyao.

Elimu hiyo  ni sehemu ya maandalizi kuelekea Maadhimisho ya Wiki ya Siku ya Haki za Mlaji Duniani 2026, yakilenga kuendelea kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa kulinda haki za walaji na kuimarisha ushindani wa haki sokoni.

Kwa ujumla, juhudi hizi zinaakisi dhamira ya Tume ya Ushindani kuhakikisha kuwa kila mlaji anakuwa na sauti, analindwa na anapata huduma bora, huku biashara zikikua katika mazingira ya haki na uwazi.

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka watayarishaji wa vipindi vya elimu kwa umma kupitia Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) wahakikishe kila wakati wanafanya utafiti na kupata takwimu sahihi.

“Maofisa Mawasiliano wote jengeni utamaduni wa kufanya tafiti, kupata takwimu sahihi kabla kuzisambaza kwa wananchi na kuhuisha taarifa za kisekta kwenye tovuti,” amesema.

Ametoa wito huo leo (Jumatano, Machi 25, 2026) mara baada ya kufungua mkutano wa 110 wa mwaka wa watayarishaji wa vipindi vya elimu kwa umma kupitia TBC uliofanyika kwenye ukumbi wa kimataifa wa PAPU (PICC) jijini Arusha. Mkutano huo unawakutanisha wadau mbalimbali wa elimu kwa umma.

Waziri Mkuu amewataka watayarishaji hao watumie vipindi walivyonavyo kutangaza mafanikio ya serikali ya awamu ya sita ili wananchi wapate taarifa sahihi. “Maofisa Mawasiliano wote tumieni kila fursa kutangaza mafanikio ya Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan katika sekta zenu ili kuwawezesha wananchi kupata taarifa sahihi za sekta mnazofanyia kazi,” amesisitiza.

Amesema kuwa ili kujihakikisha kuwa wanapata wasikilizaji na watazamaji wengi wa vipindi vyao, wanapaswa kutumia maudhui yaliyo sahihi, ya kuvutia na yenye thamani ili vijana waweze kuyapokea na kufurahia kuyafuata.

Dkt. Mwigulu amewataka watayarishaji hao waandae maudhui yatakayowafikia na kuwagusa vijana kwa lugha wanayoielewa. “Bila kutumia njia na lugha rafiki kwa vijana, taarifa muhimu zinaweza zisifikie walengwa au kushindwa kuwavutia,” amesisitiza.

Amewataka waongeze ubunifu wa kuwasaidia vijana kutambua wajibu wao katika kulinda nchi yao na tunu za taifa ili mabadiliko ya teknolojia ya habari na mawasiliano yaliyofikiwa yasitumiwe kufanya upotoshaji na kuangamiza Taifa.




 

 WAZIRI wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar, ameagiza wadau wote katika masoko ya mitaji na dhamana wazingatie sheria na kanuni za masoko ya fedha huku wakiimarisha utoaji wa huduma kwa njia ya kidigitali.

Akizungumza Jumanne wakati wa sherehe ya 5 ya kuhitimisha kozi ya Cheti cha Sekta ya Dhamana na Shindano la Vyuo Vikuu na Taasisi za Elimu ya Juu, Balozi Omar alisisitiza haja ya kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu masoko ya mitaji na dhamana ili kuongeza uelewa na ushiriki.

“Nawaasa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) na wadau kuendelea kutoa elimu kwa umma ili kuongeza uelewa na ushiriki katika sekta hii,” alisema. 

Pia aliagiza CMSA kutekeleza kikamilifu majukumu yake ya kusimamia, kuratibu na kuendeleza masoko ya mitaji na dhamana ili kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa 2050.

Balozi Omar alibainisha kwamba uelewa zaidi wa masoko ya mitaji ni muhimu ili kuhamasisha ushiriki wa Watanzania, akieleza kuwa masoko haya yana nafasi muhimu katika upatikanaji wa mitaji kwa makampuni ya umma na binafsi. Hii inawawezesha wananchi kushiriki moja kwa moja katika uchumi na kuchangia kufanikisha malengo ya Dira ya 2050.

Aliongeza kuwa, kama ilivyo kwa sekta nyingine, masoko ya mitaji na dhamana yanahitaji wataalamu wenye ujuzi na weledi wa kutosha ili kuwezesha upatikanaji wa mitaji ya muda mrefu kwa maendeleo ya uchumi wa kisasa. Alisema kuwa hadi Desemba mwaka jana, jumla ya thamani ya uwekezaji katika masoko ya mitaji ilifikia shilingi trilioni 63.15.

Awali, Mwenyekiti wa Bodi ya CMSA, Lucas Mwimo, alishukuru serikali kwa kuweka mazingira bora yanayowezesha mamlaka kukuza sekta ya masoko ya mitaji. Bw Mwimo alibainisha jitihada za CMSA kutoa mafunzo, kuanzisha bidhaa bunifu, na kuhamasisha ushiriki wa soko wa ndani na nje ya nchi.

Mkurugenzi Mtendaji wa CMSA, CPA. Nicodemus Mkama, alibainisha kuwa wahitimu wa kozi hiyo wanakidhi viwango vya kimataifa, na hivyo kuimarisha ujuzi wa wataalamu wanaotoa huduma katika masoko ya mitaji. “Kuhakikisha tunatoa elimu bora na kujenga uwezo wa wataalamu kunalingana na utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050, inayolenga kuendeleza wataalamu wenye weledi,” alisema.

CMSA pia ilianzisha Shindano la Vyuo Vikuu la Masoko ya Mitaji, lililoshirikisha wanafunzi kote nchini kupitia maswali ya mtandaoni. Jumla ya wanafunzi 28,383 walishiriki, ikizidi malengo kwa zaidi ya asilimia 140. Washindi watano wa juu walipatiwa zawadi za fedha kuanzia shilingi milioni 3 hadi 700,000, na pia watapata mafunzo nchini Nigeria pamoja na kutembelea makampuni makubwa yanayojihusisha na masoko ya mitaji.

Ili kuongeza idadi ya wataalamu waliokidhi viwango vya kimataifa, CMSA inashirikiana na Chartered Institute for Securities & Investment (CISI).

Akizungumza, Naibu Gavana  wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Yamungu Kayandabila, alisisitiza umuhimu wa ujumuishaji wa kifedha na elimu ya kifedha. “Mitandao ya kidigitali imebadilisha mfumo wa kifedha, ikiruhusu elimu ya kifedha mtandaoni. Kufunga pengo la kifedha kidijitali kati ya vijijini na mijini ni jambo kuu katika sera yetu ya fedha na mfumo wa kitaifa wa ubunifu wa kifedha,” alisema.



Kaimu Katibu Tawala wa  Mkoa wa Mara  Dkt.Zabron Masatu akizungumza na maafisa wa TASAC waliotembelea Ofisi ya Mkoa wa Mara.




Na Mwandishi Wetu
SERIKALI ya Mkoa wa Mara imewataka Wavuvi na wamiliki wa vyombo vidogo vya majini kulazimisha safari za majini pindi wanapoona viashiria vya hatari ya hali ya hewa katika kipindi hiki cha mvua.

Hayo ameyasema Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Mara, Dkt. Zabron Masatu wakati akizungumza na maafisa wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) walioko katika zoezi la kutoa elimu ya usalama majini.

Dkt.Masatu amesema kuwa ni wajibu wa kila mmiliki, mvuvi na wasafirishaji kuhakikisha usalama wa maisha unatangulizwa mbele ya tamaa ya kipato. Ameeleza kuwa mara nyingi ajali hutokea kwa sababu ya kupuuza viashiria vya hatari, ikiwemo taarifa za hali ya hewa ikiwemo mawimbi makali, mvua kubwa na upepo mkali unaoambatana na msimu huu mvua za masika.

“Ni bora kuchelewesha safari kuliko kupoteza maisha,” amesisitiza.

Kwa upande wao, Afisa Mfawidhi wa Mkoa wa Mara, Hezron Lusangija pamoja Afisa Uvuvi wa Wilaya ya Rorya, Godfrey Bwatondi, wameendelea kutoa elimu kwa wavuvi na wananchi kuhusu matumizi sahihi ya vifaa okozi, hususan maboya (life jackets), wakieleza kuwa vifaa hivyo si mzigo bali ni kinga ya uhai wawapo kwenye shughuli mbalimbali za kusafiri au kuvua. Wamesema kuwa kumekuwa na dhana potofu miongoni mwa baadhi ya wavuvi kwamba kuvaa jaketi okozi kunawapa usumbufu, jambo ambalo ni linahatarisha maisha yao mara ajali inapotokea kwa vyombo vidogo.

TASAC imeeleza kuwa kampeni ya elimu ya usalama majini inalenga kuwakumbusha wadau wote kufuata Sheria na taratibu zilizowekwa, ikiwemo kuhakikisha kila chombo kinachoingia majini kinakuwa na maboya yenye idadi inayolingana na abiria. Elimu hiyo pia inalenga kuondoa tabia ya wavuvi na wananchi kuvaa maboya vibaya au kuvua mara wanapofika majini, wakijiamini kuwa uwezo wa kuogelea unatosha au watavaa mara ajali itakapotokea, kitu ambacho hakiwezekani pale inapotokea.

Wananchi wa Rorya na maeneo jirani wamepongeza juhudi hizi, wakisema elimu inayotolewa imekuwa msaada mkubwa katika kuimarisha usalama na kupunguza ajali. Wamesema kuwa kampeni hii imewasaidia kuelewa kuwa jaketi okozi ni ngao ya uhai na si mzigo wa gharama.

Serikali ya Mkoa wa Mara imesisitiza kuwa itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wakiwemo TASAC ili kuhakikisha usalama wa wananchi unakuwa kipaumbele, na kwamba hakuna maisha yanayopaswa kupotea kwa sababu ya uzembe au kupuuza tahadhari za hali ya hewa

Na Mwandishi Wetu

Dodoma — Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira Tanzania limetangaza kushiriki rasmi mkutano wa wadau wa Tiba Asilia na Tiba Mbadala unaoandaliwa na Wizara ya Afya Tanzania, utakaofanyika Machi 25, 2026 katika Mji wa Serikali Mtumba, wilayani Chamwino, jijini Dodoma.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mwenyekiti wa shirika hilo, Simba A. Simba, mkutano huo unachukuliwa kuwa fursa ya kihistoria kwa wadau wa sekta ya tiba asilia kukutana, kubadilishana mawazo na kuweka mikakati ya pamoja itakayosaidia kuimarisha sekta hiyo nchini.

Amesema kuwa mkutano huo ni hatua muhimu katika kujenga mustakabali wa Tiba Asilia kwa kuzingatia misingi ya ubora, uwajibikaji, heshima na utambuzi wa kitaifa na kimataifa.

“Tiba Asilia haiwezi kutenganishwa na mazingira, kwani rasilimali zake zinatokana na bioanuwai ya nchi. Hivyo, ulinzi wa mazingira ni msingi wa uendelevu wa sekta hii,” alisema Simba.

Aliongeza kuwa mabadiliko ya tabianchi na uharibifu wa mazingira vinaathiri moja kwa moja upatikanaji wa dawa asilia, hivyo kuna umuhimu wa kuweka mikakati madhubuti ya uhifadhi na matumizi endelevu ya rasilimali hizo.

Aidha, shirika hilo limeeleza kuwa katika dunia ya sasa yenye changamoto za magonjwa ya kuambukiza na yasiyo ya kuambukiza, Tiba Asilia ina nafasi muhimu ya kuwa sehemu ya suluhisho endapo itaendelezwa kisayansi na kusimamiwa kwa weledi.

Katika mkutano huo, wadau wanatarajiwa kujadili pia namna ya kuunganisha maarifa ya jadi na sayansi ya kisasa, pamoja na kutumia teknolojia mpya ikiwemo Akili Unde (AI) katika utafiti na uhifadhi wa tiba asilia.

Shirika hilo pia limehimiza umuhimu wa ushirikishwaji mpana wa wadau wote, wakiwemo serikali, sekta binafsi, vyuo vikuu na mashirika ya kijamii, ili kujenga mfumo imara wa kitaasisi utakaoongeza uwajibikaji na ufanisi wa sekta hiyo.

Sambamba na hilo, limependekeza kuimarishwa kwa ujumuishaji wa Tiba Asilia katika mifumo rasmi ya afya, ikiwemo kuingizwa kwenye Bima ya Afya, upatikanaji wa dawa kupitia Bohari ya Dawa (TMSD), pamoja na kuongeza uwekezaji katika tafiti na ubunifu.

Aidha, shirika hilo limebainisha kuwa Tiba Asilia ina uwezo mkubwa wa kuchangia uchumi wa taifa kupitia ajira na mapato, hivyo kuna haja ya kuweka mazingira rafiki ya uwekezaji na upatikanaji wa mitaji kwa wadau wa sekta hiyo.

Kwa upande mwingine, wadau wamehimizwa kutumia mkutano huo kujenga umoja, kuondoa tofauti zisizo za msingi na kupambana na vitendo vinavyochafua taswira ya sekta, ikiwemo ulaghai na huduma zisizo na weledi.

Mkutano huo unatarajiwa kuwa jukwaa muhimu la kuweka dira mpya ya maendeleo ya Tiba Asilia nchini, huku wadau wakihimizwa kushiriki kikamilifu kwa manufaa ya taifa.
Huu ni wakati wa kuunganisha nguvu, hekima na uzoefu wetu kwa manufaa ya taifa letu. Muda ni sasa. Tunawahimiza wadau wote kujitokeza kwa wingi na kushiriki kikamilifu katika mkutano huu muhimu.

Imetolewa na: Simba A. Simba Mwenyekiti Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira Tanzania

Tarehe: 24 Machi 2026

Na. OWM- KAM

‎Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Rahma Kisuo amewataka wataalamu na wadau wa Ustawi wa Jamii kufanya kazi kwa weledi, uadilifu katika utendaji kazi hususani kwa watoto na wananchi wanyonge.

Ameyasema hayo Machi 24, 2026 Jijini Dodoma wakati alipofungua Kongamano na Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Wataalamu wa Ustawi wa Jamii Tanzania (TASWO) huku akiwasisitiza wataalam hao kutumia teknolojia (mifumo ya Kielektroniki) katika utendaji kazi ili kurahisisha ukusanyaji wa taarifa mbalimbali.

‎Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama wa wataalamu wa Ustawi wa Jamii (TASWO) Dkt. Mariana Makuu akizungumza kwenye kikao hicho alisema kongamano limelenga kuwakutanisha wanataaluma wa huduma za ustawi wa jamii, watunga sera ,wanafunzi na wakufunzi kutoka vyuo vinavyotoa taaluma za ustawi wa jamii ili kujadili kwa pamoja maswala ya kitaalamu kwa lengo kuu la kuboresha elimu ,sera na huduma za utawi wa nchi.




Na Mwandishi Wetu.

Katika hatua ya kuondoa mzigo wa gharama za matibabu kwa wananchi, Serikali imezindua utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Bima ya Afya kwa Wote, utakaowezesha familia ya watu sita kupata huduma za afya 372 kwa gharama ya Sh 150,000 kwa mwaka.

Kwa mujibu wa Mratibu wa Elimu kwa Umma wa Mpango wa Taifa wa Bima ya Afya kwa Wote, Said Makora, mpango huo ni sehemu ya mkakati wa Serikali kuhakikisha huduma za afya zinawafikia wananchi wote bila kujali uwezo wao wa kifedha.

Amesema kupitia mpango huo, huduma zitakazotolewa zinajumuisha uchunguzi wa maabara, radiolojia, dawa na vifaa tiba pamoja na upasuaji mdogo na mkubwa, kuanzia ngazi ya zahanati hadi hospitali za rufaa za taifa.

Makora alibainisha kuwa Serikali kupitia Wizara ya Fedha imeweka vyanzo maalum vya mapato vitakavyokusanya takribani Sh bilioni 201.9 katika mwaka wa fedha 2025/2026 ili kugharamia wananchi wasio na uwezo, huku zaidi ya Sh bilioni 48.2 zikiwa tayari zimekusanywa katika robo ya kwanza ambazo zitakazonufaisha kaya laki 276.

Aliongeza kuwa mpango huo pia unalenga kupunguza vifo vinavyoweza kuzuilika kwa kuimarisha huduma za afya ya mama na mtoto pamoja na kudhibiti magonjwa yanayoongoza kuathiri wananchi kama malaria, kifua kikuu na UKIMWI.

Kuhusu walengwa wa mpango huo, alisema tayari zaidi ya kaya 931,000 zimetambuliwa kupitia kanzidata ya TASAF, huku Serikali ikilenga kufikia zaidi ya kaya milioni 3.9 zitakazonufaika na mpango huo, gharama zao zikigharamiwa kikamilifu.

“Mpango huu unakwenda kubadili maisha ya wananchi kwa kuhakikisha wanapata huduma za afya kwa wakati bila hofu ya gharama,” alisema Makora.

Utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote unatarajiwa kuongeza usawa katika upatikanaji wa huduma za afya, kupunguza umasikini unaosababishwa na gharama za matibabu na kuimarisha ustawi wa jamii kwa ujumla.

Wanawake wajasiriamali kutoka mikoa mbalimbali nchini wamejengewa uwezo kupitia mradi wa Women Creating Wealth (WCW) unaotekelezwa na Shirika la Graca Machel Trust, ukiwa na lengo la kuwawezesha kujikwamua kiuchumi na kukuza mitaji yao ya kibiashara.

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam katika mahafali ya wahitimu wa mradi huo, Mratibu wa Women Creating Wealth (WCW), Angaja Mwanga amesema kuwa hadi sasa mradi huo umefanikiwa kuwafikia wanawake wajasiriamali zaidi ya 10,000, hatua inayotarajiwa kuchochea ukuaji wa uchumi wao binafsi pamoja na kuwasaidia kufikia masoko mapana zaidi.

Kwa upande wake, mtoa mada wa mradi huo, Fatma Abdallah Kange amesema wanawake wengi katika jamii wanakabiliwa na changamoto za ukosefu wa ujuzi na uzoefu wa kibiashara, hivyo mafunzo yanayotolewa kupitia mradi huo yanalenga kuziba pengo hilo na kuwawezesha kufanya biashara kwa ufanisi.

Nao baadhi ya wahitimu wa mradi huo, akiwemo Asimin Gombo na Mectlida Godfrey, wameeleza kuwa mafunzo waliyopata yamewajengea uwezo mkubwa wa kuendesha na kukuza biashara zao, pamoja na kuwasaidia kutafuta na kupanua masoko.







Top News