no image

Vijana katika mikoa tisa nchini wanatarajiwa kunufaika na Programu ya Mifumo Himilivu ya Chakula inayotekelezwa na Wizara ya Kilimo kwa lengo la kuongeza ushiriki wao katika sekta ya kilimo kupitia matumizi ya teknolojia za kisasa na miradi ya umwagiliaji inayotarajiwa kuanza mwaka ujao.

Akizungumza na waandishi wa habari Juni 22, 2026, wakati wa Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma jijini Dodoma, Mtaalamu wa Masuala ya Vijana, Laurean Masele, amesema programu hiyo inalenga kuwajengea vijana uwezo wa kujiajiri na kuongeza kipato kupitia kilimo chenye tija.

Amesema mikoa inayonufaika na programu hiyo ni Tanga, Arusha, Kilimanjaro, Dodoma, Pwani, Morogoro, Njombe, Iringa na Mbeya, ambapo vijana wanahamasishwa kujiunga na shughuli za kilimo cha kisasa kupitia halmashauri za maeneo husika.

Masele amesema programu hiyo imeweka mkazo kwenye kilimo cha mazao ya bustani kama nyanya na vitunguu ambavyo hukomaa kwa muda mfupi na kuwawezesha vijana kupata kipato kwa haraka.

Aidha, utekelezaji wa skimu za umwagiliaji pamoja na uchimbaji wa visima kwa wakulima wadogo unatarajiwa kuongeza upatikanaji wa maji kwa shughuli za kilimo na kuifanya sekta hiyo kuwa ya kuvutia zaidi kwa vijana.

Ameeleza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya juhudi za serikali za kubadilisha mtazamo wa vijana kuhusu kilimo na kukifanya kuwa chanzo muhimu cha ajira na maendeleo ya kiuchumi.

 





Asema mambo ya kutegemea wahisani yamepitwa na wakati
WAZIRI Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka Watanzania kushirikiana na Serikali katika kutunza na kuhudumia vituo vya watoto wenye mahitaji maalumu na wasiojiweza badala ya kutegemea wahisani kutoka nje kwani mambo hayo yamepitwa na wakati.

Ametoa kauli hiyo leo Jumapili, Juni 21, 2026 katika harambee ya uchangiaji wa jengo la kitega uchumi cha kanisa la Anglika jijini Dodoma. “Mambo ya misaada yamepitwa na wakati na hata katika bajeti Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameendelea kusisitiza kuwa na bajeti ya nchi ambayo inategemea rasilimali za ndani ya nchi”.

Pia, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu ametoa rai halmashauri zote nchini ziandae orodha ya vituo vya kulelea watoto wenye mahitaji maalumu na wasiojiweza na kuona namna ya kuvisaidia ambapo amesisitiza si vema kuwaandikia watu hao barua za kwenda kuomba misaada pindi wanapofika kwenye ofisi za umma.

Waziri Mkuu amesema awali katika maeneo mbalimbali nchini ilizoeleka kuwa vituo vya kulelea watoto yatima na wenye mahitaji maalumu viliendeshwa kupitia misaada kutoka nje ya nchi dhana ambayo watu wanatakiwa kuachana nayo.

Kadhalika, Waziri Mkuu ametumia fursa hiyo kuwahimiza Watanzania kuendelea kusimama katika mafundisho mbalimbali yanayotolewa na viongozi wa dini ikiwemo kuendeleza amani na umoja wa kitaifa.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan analipongeza Kanisa la Anglikana Tanzania kwa kuendeleza mradi wa ujenzi wa kitega uchumi kwa sababu ukuaji wa uchumi ni miongoni mwa malengo muhimu ya maendeleo.

Awali, Katibu Mkuu wa Kanisa la Anglikana Tanzania, Kasisi Canon Dkt. George Lawi alisema ili kuimarisha uwezo wa kifedha na kupunguza utegemezi, Kanisa la Anglikana Tanzania lilianzisha mradi wa kitega uchumi jijini Dodoma na kuhakikisha linakuwa na vyanzo endelevu vya mapato vitakavyowezesha utekelezaji wa majukumu ya kiroho na kijamii kwa ufanisi zaidi.

Alisema jengo hilo linatarajiwa kutoa huduma mbalimbali zikiwezo za hoteli, ofisi na hivyo kuchangia katika kukuza uchumi wa kanisa na Taifa kwa ujumla. “Mradi huu umefikia hatua ya umaliziaji na umeshagharimu shilingi bilioni tatu na bado zinahitajika shilingi bilioni 1.5 ili kukamilisha na ndiyo sababu ya kufanya harambee leo.”

Pia, Dkt. Lawi alitumia fursa hiyo kumuahidi Waziri Mkuu kuwa Kanisa Anglikana Tanzania litaendelea kuwa mshirika wa Serikali katika juhudi za kuwaletea wananchi maendeleo endelevu kupitia sekta za elimu, afya, uwezeshaji wa jamii na kukuza maadili mema.

Katika harambee hiyo zaidi ya shilingi bilioni moja zilipatikana, ambapo pia Kanisa Anglikana limempa Heshima ya Kikanisa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa Lay Canon, mshauri wa mambo ya Kanisa baada ya kuridhishwa na utendaji wake.




 





Na Oscar Assenga,TANGA.

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Wazo Michael Mwang’onda, amepongeza utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa miundombinu ya kuboresha upatikanaji wa maji safi katika eneo la Mzizima hadi Mikocheni, akisema unadhihirisha dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kusogeza huduma muhimu karibu na wananchi.

Mwenge wa Uhuru 2026 umetembelea na kukagua mradi huo unaotekelezwa na Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Tanga (Tanga UWASA) katika Kata ya Mzizima, ambapo viongozi wa mbio hizo walieleza kuridhishwa na kasi ya utekelezaji wake.


Akizungumza baada ya ukaguzi huo na kushiriki katika zoezi la kumuunganishia mteja mpya huduma ya maji safi, Mwang’onda alisema Serikali chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kutekeleza mkakati wa kuboresha huduma za maji nchini ili kumtua mama ndoo kichwani.

Alisema dhamira hiyo inaonekana kupitia miradi mbalimbali ya kimkakati inayotekelezwa katika sekta ya maji nchini, huku akiipongeza Tanga UWASA kwa usimamizi mzuri wa mradi huo ambao unalenga kuongeza upatikanaji wa huduma ya maji kwa wananchi.

Kwa upande wake, Msimamizi wa Mradi, Mhandisi Aaron Chanimbaga, akisoma taarifa ya utekelezaji alisema mradi huo wenye thamani ya Shilingi milioni 233.4 umefikia asilimia 50 ya utekelezaji.

Alieleza kuwa mradi huo unatarajiwa kukamilika ifikapo Septemba mwaka huu na unalenga kunufaisha zaidi ya wananchi 4,780 kwa kuwapatia huduma ya maji safi na salama kwa uhakika.

Mbio za Mwenge wa Uhuru 2026 zinaongozwa na kauli mbiu isemayo: “Tanzania ni yetu sote, tushirikiane kwa pamoja kuleta maendeleo.”










Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma

Serikali imesisitiza dhamira yake ya kuwatambua na kuwawezesha vijana nchini kwa kuimarisha mifumo ya ukusanyaji wa takwimu na kuongeza fursa za kiuchumi na kijamii kwa kundi hilo muhimu la maendeleo ya taifa.

Akijibu swali bungeni leo lililoulizwa na Mbunge wa Viti Maalum, Latifa Khamis Juwakali, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana, Joel Nanauka, amesema Serikali inalitambua kundi la vijana kama nguzo muhimu ya maendeleo ya nchi.

Waziri Nanauka amesema Serikali imechukua hatua mbalimbali za kuhakikisha vijana wanatambuliwa rasmi kupitia zoezi la Utambuzi wa Vijana (Youth Mapping) linaloratibiwa na Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana.

Ameeleza kuwa zoezi hilo litasaidia kupata takwimu sahihi kuhusu idadi ya vijana, mahitaji yao halisi, pamoja na changamoto zinazowakabili, hatua itakayosaidia kupanga na kutekeleza afua zenye tija zaidi katika nyanja za kiuchumi na kijamii.

Aidha, Serikali imeendelea kutekeleza programu mbalimbali za uwezeshaji vijana kupitia wizara za kisekta, mashirika ya umma, sekta binafsi na wadau wa maendeleo ili kuhakikisha vijana wanapata fursa za kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo.

Katika hatua nyingine, Waziri huyo amebainisha kuwa Serikali imeweka mifumo ya upatikanaji wa mitaji yenye masharti nafuu, ikiwemo Mfuko wa Maendeleo ya Vijana pamoja na mikopo inayotokana na asilimia 4 ya mapato ya ndani ya Halmashauri, ambayo hutengwa mahsusi kwa ajili ya kuwawezesha vijana kiuchumi.

Serikali imesisitiza kuwa itaendelea kuimarisha programu hizo ili kuhakikisha vijana wanakuwa sehemu muhimu ya ukuaji wa uchumi na maendeleo endelevu ya taifa.



Na Janeth Raphael MichuziTv

RAIS wa Namibia, Netumbo Nandi-Ndaitwah, ametembelea Kituo cha Kumbukumbu cha Wapigania Uhuru wa Afrika pamoja na Makaburi ya Mashujaa wa Namibia yaliyopo wilayani Kongwa mkoani Dodoma, katika ziara maalum ya kuenzi mchango wa Tanzania katika harakati za ukombozi wa bara la Afrika.

Katika ziara hiyo yenye umuhimu mkubwa wa kihistoria, Rais Nandi-Ndaitwah ameongozana na ujumbe wa viongozi waandamizi kutoka Namibia, ukiwemo mawaziri, wabunge na maafisa mbalimbali wa serikali. Upande wa Tanzania, viongozi kadhaa wa Serikali walishiriki katika mapokezi hayo, akiwemo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Profesa Palamagamba Kabudi, pamoja na Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Paul Makonda.

Akiwa katika eneo hilo la kihistoria, Rais wa Namibia aliongoza shughuli ya uwekaji mashada ya maua katika makaburi ya wapigania uhuru wa Namibia waliopoteza maisha wakati wa mapambano dhidi ya ukoloni, kama ishara ya heshima na kumbukumbu kwa mchango wao katika kuipigania nchi yao.

Akizungumza baada ya shughuli hiyo, Rais Nandi-Ndaitwah alisema Kongwa ina nafasi ya pekee katika historia ya Namibia kutokana na mchango wake katika harakati za ukombozi, akisisitiza kuwa taifa lake litaendelea kuthamini na kukumbuka msaada mkubwa uliotolewa na Tanzania katika kipindi hicho muhimu.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa Tanzania na Namibia kuimarisha ushirikiano wao katika nyanja za maendeleo na uchumi, akieleza kuwa baada ya ushindi wa kisiasa, mataifa ya Afrika yanapaswa kuelekeza nguvu katika kupigania uhuru wa kiuchumi kwa manufaa ya wananchi wake.

Rais huyo pia alieleza kuwa uhusiano kati ya Tanzania na Namibia umejengwa juu ya misingi imara ya historia, mshikamano na damu ya mashujaa waliopigania uhuru, akibainisha kuwa urithi huo utaendelea kuwa daraja muhimu linalounganisha mataifa hayo mawili kwa vizazi vijavyo.

Ziara ya Rais Nandi-Ndaitwah nchini Tanzania inatazamwa kama hatua mpya ya kuimarisha ushirikiano wa kimkakati kati ya nchi hizo mbili, huku ikitarajiwa kufungua fursa zaidi katika sekta za biashara, uwekezaji, utamaduni na diplomasia kwa manufaa ya pande zote.







Uwepo wa viwanda umekuwa kichocheo muhimu cha ukuaji wa uchumi kwa kuongeza vyanzo vya mapato kwa Serikali za Mitaa na Serikali Kuu kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Hadi kufikia Machi 2026, Mkoa wa Pwani ulikadiria kukusanya Sh bilioni 189.645 kutoka kodi za ndani na forodha, lakini ulifanikiwa kukusanya Sh bilioni 216.029 sawa na asilimia 113.91 ya lengo.

Kadhalika, Mkoa wa Pwani ulilenga kukusanya Sh bilioni 88 za mapato ya ndani, lakini kufikia Aprili 2026 makusanyo yalikuwa yamefikia bilioni 94 huku hadi Mei yakifikia bilioni 114.5.

Mafanikio hayo ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2025/2030, yakionyesha usimamizi madhubuti wa Serikali katika kuimarisha uwekezaji, viwanda, bandari, barabara, umeme na miundombinu mingine, ambayo imeendelea kuchochea ukuaji wa uchumi na kuleta maendeleo. 







 

Leo tumefungua rasmi ziara ya Kamati ya Utekelezaji ya Jumuiya ya Wazazi Mkoa wa Dar es Salaam  katika Jimbo la Ubungo Jana

Akizungumza na viongozi wa Kata na Matawi, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Mkoa wa Dar es Salaam, Khadija Ally, amewashukuru kwa moyo wa kujitolea, uzalendo, mshikamano na ushiriki wao wa hali na mali katika kufanikisha shughuli za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.

“Uzalendo wenu, mshikamano wenu, kujitolea kwenu na imani yenu kwa Chama Cha Mapinduzi vimechangia kwa kiwango kikubwa mafanikio ya chama na ushindi uliopatikana.”

Ziara hii inalenga kuwashukuru viongozi na wanachama wetu, kuimarisha umoja na mshikamano, pamoja na kuhamasisha ari ya utendaji kazi katika kuendelea kuijenga Jumuiya ya Wazazi na Chama Cha Mapinduzi kwa maendeleo ya Taifa letu.
Katika ziara hii, Kamati ya Utekelezaji ya Mkoa wa Dar es Salaam chini ya Mwenyekiti wake Khadija Ally itatembelea Kata zote 102 za Mkoa wa Dar es Salaam na kugawa tuzo za pongezi na shukrani kwa viongozi wa Kata kwa mchango wao mkubwa katika kuimarisha chama.

Tunawathamini, tunawapenda, na tunaamini kuwa nguvu ya Chama Cha Mapinduzi ipo kwa wanachama wake wenye uzalendo, uaminifu, mshikamano na imani thabiti kwa chama chao.

#JumuiyaYaWazaziDSM
#UmojaMshikamanoNaMaendeleo
#CCMKaziIendelee
#ZiaraYaShukrani2026





 

Na Belinda Joseph- Dodoma.

Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) umeendelea kuwa nguzo muhimu katika kusogeza huduma za mawasiliano karibu na wananchi, hususan waishio maeneo ya vijijini yasiyo na mvuto wa kibiashara kwa kampuni za mawasiliano.

Akizungumza wakati wa maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, Mhandisi Wilfred Charles kutoka UCSAF Juni 21, 2026, amesema ushiriki wao katika maadhimisho hayo unalenga kuielimisha jamii kuhusu majukumu na miradi mbalimbali inayotekelezwa na mfuko huo katika kuboresha huduma za mawasiliano nchini.

Amesema UCSAF kwa kushirikiana na Serikali imekuwa ikitoa ruzuku kwa watoa huduma za mawasiliano ili kuhakikisha huduma hizo zinafika katika maeneo ya vijijini ambayo kwa kawaida hayavutii uwekezaji wa kibiashara.

Ameeleza kuwa Mbali na ujenzi wa miundombinu ya mawasiliano, UCSAF pia inatekeleza mradi wa utoaji wa huduma za WiFi katika maeneo ya wazi, pamoja na kupanua usikivu wa Redio ya Taifa na redio za kijamii katika maeneo mbalimbali nchini, hatua hiyo inalenga kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi na huduma za habari kwa urahisi zaidi.

Katika sekta ya elimu, UCSAF imefanikiwa kufikisha vifaa vya TEHAMA katika shule zaidi ya 1,000 za msingi, sekondari na vyuo nchini, ambazo zimeunganishwa na huduma ya intaneti huku wanafunzi wakipatiwa kompyuta ili kuwajengea uwezo wa kutumia teknolojia za kidigitali na kuongeza ushindani wao katika uchumi wa kidigiti.

Aidha, amesema mfuko huo unaendelea kutoa mafunzo ya TEHAMA kwa walimu ili kuwawezesha kufundisha kwa ufanisi zaidi masomo yanayohusiana na teknolojia pamoja na kutumia mifumo ya kidigitali katika utekelezaji wa majukumu yao.

Mhandisi Charles amesema juhudi hizo zinaendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, hususan lengo la nne ambalo linaweka mkazo katika matumizi ya TEHAMA na kuongeza upatikanaji wa huduma za serikali kwa wananchi wa maeneo ya vijijini.

Kwa upande wa mafanikio ya mawasiliano, amebainisha kuwa tangu kuanzishwa kwa UCSAF, zaidi ya minara 2,000 ya mawasiliano imejengwa katika maeneo ya vijijini, pia mradi wa ujenzi wa minara 758 uliokamilika na kuzinduliwa na Rais Samia Suluhu Hassan umewezesha zaidi ya wananchi milioni 8.5 kupata huduma za mawasiliano.

Sambamba na hilo, UCSAF imeboresha teknolojia ya mawasiliano kwa kupandisha hadhi ya minara 304 iliyokuwa ikitoa huduma za 2G pekee na kuiwezesha kutoa huduma za 3G na 4G, hatua iliyoongeza kasi na ubora wa mawasiliano kwa wananchi wengi zaidi.

Mhandisi Charles amewakaribisha wananchi kutembelea banda la UCSAF katika maadhimisho hayo ili kupata elimu kuhusu huduma zinazotolewa na mfuko huo, pamoja na kutoa taarifa za maeneo ambayo bado hayajafikiwa na huduma za mawasiliano.

"Malengo yetu ni kuhakikisha kila Mtanzania, awe wa mjini au kijijini, anapata huduma bora za mawasiliano kwa usawa".


Zaidi ya wananchi 300 wametembelea banda la Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) tangu kuanza kwa Wiki ya Utumishi wa Umma, wakipata elimu na ufafanuzi kuhusu utekelezaji wa miradi mbalimbali ya barabara katika maeneo yao, hatua hiyo imeendelea kuimarisha uhusiano kati ya wananchi na taasisi hiyo huku ikitoa fursa ya kusikiliza na kutatua changamoto zinazowakabili wananchi moja kwa moja.

Akizungumza katika maonesho hayo, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano kwa Umma wa TARURA, Catherine Sungura, amesema wananchi wanaowasilisha kero zao huunganishwa moja kwa moja na mameneja wa maeneo husika ili kupata maelezo ya kina pamoja na ufumbuzi wa haraka, ameeleza lengo ni kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi kuhusu miradi inayotekelezwa na maendeleo yake.

Katika mwendelezo wa Wiki ya Utumishi wa Umma unaoendelea Jijini Dodoma hadi Juni 23, Sungura alieleza kuwa mwananchi kutoka eneo la Kimara amewasilisha maswali kuhusu maendeleo ya miundombinu ya barabara katika eneo lao , amesema TARURA imekuwa ikitoa ufafanuzi wa kina kwa kila mwananchi anayefika kwenye banda hilo.

Akizungumzia barabara ya King'ong'o iliyopo Kimara, Wilaya ya Ubungo jijini Dar es Salaam, Sungura amesema ujenzi wa barabara ya zege unaoanzia eneo la TRA kuelekea King'ong'o unaendelea vizuri, amebainisha kuwa amewasiliana na Meneja wa TARURA Wilaya ya Ubungo na amewahakikishia wananchi kuwa kilomita 1.6 pekee ndizo zimebaki kukamilishwa, huku mita 800 zikitarajiwa kujengwa mwanzoni mwa mwaka mpya wa fedha kuanzia Julai na sehemu iliyobaki kukamilishwa katika awamu inayofuata.

Amesisitiza kuwa TARURA itaendelea kuhakikisha miundombinu ya barabara inaboreshwa ili kurahisisha mawasiliano na usafiri kwa wananchi, huku akieleza kuwa barabara bora zinachochea upatikanaji wa huduma za kijamii, biashara na shughuli nyingine za maendeleo jambo ambalo ni muhimu katika kuinua ustawi wa jamii na kukuza uchumi wa maeneo mbalimbali nchini.


Wananchi nchini wametakiwa kuwa waangalifu na taarifa pamoja na ushauri wanaoupata kupitia mitandao ya kijamii, kwani si kila elimu inayotolewa mtandaoni ni sahihi au inatolewa na wataalamu wenye sifa stahiki.

Wito huo umetolewa na Mkuu wa Chuo cha Ustawi wa Jamii, Dkt. Joyce Nyoni, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma Juni 21, 2026, katika mwendelezo wa maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma.

Dkt. Nyoni amesema kumekuwa na ongezeko la watu wanaotoa ushauri na elimu mbalimbali mtandaoni bila kuwa na taaluma husika, jambo ambalo linaweza kuwasababisha wananchi kupata huduma zisizo sahihi na hatimaye kufanya hali zao kuwa mbaya zaidi.

Amesisitiza kuwa wananchi wanapaswa kutafuta huduma na ushauri kutoka kwa wataalamu waliopo katika mifumo rasmi ya serikali na taasisi zinazotambulika ili kuhakikisha wanapata msaada unaozingatia misingi ya kitaalamu.

Akizungumzia nafasi ya chuo hicho, Dkt. Nyoni amesema Chuo cha Ustawi wa Jamii kinaendelea kutoa mafunzo katika taaluma za ustawi wa jamii na saikolojia, huku kikizalisha wataalamu mahiri wanaoweza kusaidia jamii kukabiliana na changamoto mbalimbali za kijamii na kisaikolojia.

Ameeleza kuwa wanafunzi wa chuo hicho hujengewa uwezo wa kitaaluma na vitendo kupitia ushiriki wao katika matukio mbalimbali ya kijamii pamoja na majanga, hatua inayowasaidia kuwa wataalamu wenye uzoefu wa kutosha katika kutoa huduma kwa jamii.

Aidha, amesema katika kila ngazi ya utawala kuanzia kata hadi taifa kuna maafisa ustawi wa jamii ambao wananchi wanaweza kuwafikia kwa ajili ya kupata ushauri na huduma stahiki zinazoweza kuwasaidia kujenga maisha bora na kutatua changamoto wanazokabiliana nazo.

Dkt. Nyoni pia amesema Chuo cha Ustawi wa Jamii, kilicho chini ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, kinaendelea na zoezi la udahili kwa wanafunzi wanaotaka kujiunga na masomo mbalimbali yanayotolewa chuoni hapo.

Ametoa rai kwa vijana na wananchi wenye sifa kutumia fursa hiyo kujiunga na chuo hicho ili kupata elimu na ujuzi utakaowawezesha kuwa sehemu ya wataalamu wanaochangia ustawi wa jamii na maendeleo ya taifa.







Na Seif Mangwangi, Michuzi TV Arusha

WANAFUNZI wanaofanya ubunifu wa matumizi ya teknolojia mbalimbali katika chuo cha ufundi Arusha (ATC), wametakiwa kusoma Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kuielewa na kuona fursa zilizopo ndani yake na kufanya bunifu zao kutokana na malengo ya dira hiyo.

Hayo yameelezwa Juni 19, 2026 na Mkuu wa chuo cha ufundi Arusha Profesa Musa Chacha katika hotuba yake ya kufungua wiki ya maonyesho ya ubunifu yanayoandaliwa kila mwaka chuoni hapo.

Profesa Chacha amesema dira ya Taifa 2050 imeainisha maeneo ambayo yanapaswa kuendelezwa kwaajili ya Maendeleo ya Watanzania hivyo wanafunzi wanaofanya bunifu chuoni hapo wanapaswa kuyasoma na kuyajua na kuyafanyia ubunifu.

Amesema kutokana na kazi nzuri ya ubunifu ambayo imekuwa ikifanywa na wanafunzi chuoni hapo, chuo kimepanga kujenga jengo maalum la ghorofa nne ambalo litatumika kwaajili ya shughuli za ubunifu.

“ Kwa kushirikiana na Serikali ya Italia hivi karibuni tunatarajia kujenga jengo kubwa la ghorofa nne ambalo litatumika kwaajili ya shughuli za ubunifu( innovation), hapa chuoni hatutaki hivi vipaji vyenu vipotee,” amesema.

Aidha Profesa Chacha amesema chuo kinaendelea na ujenzi wa karakana ( industrial workshop), ambayo itatumika kutengeneza mitambo bunifu itakayokuwa ikigunduliwa na wanafunzi chuoni hapo kwaajili ya kuuzwa na kwamba tayari mashine zitakazotumika katika karakana hiyo zipo njiani kufika chuoni hapo.

“ Hivi sasa tumeamua kuendeleza bunifu zote zitakazobuniwa na wanafunzi Kwa kuzizalisha na kuziingiza sokoni, tutakuwa na kiwanda hapa hapa chuoni na wote mnaofanya ugunduzi huu tutaendelea kuwafuatilia na kuona namna mnafaidika na bunifu zenu, tutawashika mkono popote mtakapoenda,” amesema Profesa Chacha.

Aidha amesema chuo kinakamilisha jengo la hospitali itakayokuwa ikitibia wanafunzi chuoni hapo lakini pia chuo kipi kwenye mikakati ya kujenga jengo litakalojulikana kama innovation center ambalo litakuwa maalum kwaajili ya ugunduzi na uzalishaji wa vifaa tiba vya hospitalini ( biomedical engineering).

Awali akimkaribisha mgeni rasmi Makamu mkuu wa chuo, Dkt Yusuph Mhando alisema katika maonyesho ya mwaka huu ambayo ni awamu ya tatu tangu kuanzishwa, jumla ya bunifu 75 ziliingia kwenye ushindani.

Amesema kati ya bunifu hizo, bunifu 20 zilihusiana na teknolojia ya habari na mawasiliano(Tehama), umeme 15, mitambo na magari 19, sayansi timizi 8, ujenzi na barabara13 na kwamba baada ya majaji kupitia bunifu hizo jumla ya bunifu 19 pekee ziliweza kuingia fainali.

Amesema mshindi wa kwanza ametoka katika fani ya mitambo aliyegundua mashine inayojulikana kama ( Energy trauma kit), akifuatiwa na Tehama ambaye amegundua mashine ya kupima uoni wa macho ( VR acute test),

Aidha amesema maonyesho hayo ni muhimu Kwa Taifa Kwa kuwa yamekuwa yakikuza ujuzi wa wanafunzi chuoni hapo Kwa kuweza kuonyesha Kwa vitendo kile ambacho wamekuwa wakifundishwa darasani.

“ Katika bunifu hizi, Kuna vijana wametengeneza mfumo wa kupiga kura wakati wa uchaguzi ukiwa nyumbani, teknolojia hii ikiweza kuboresha itaweza kusaidia sana katika eneo hili,” amesema.

Amesema ni tegemeo la chuo kuwa bunifu hizo zitafikia jamii na kutatua kero mbalimbali inazizikabili na hivyo chuo kitaendelea kuimarisha na kuendeleza vipaji vya wanafunzi hao.



 

Tume ya Ushindani (FCC) imesema imeanza mpango wa kuanzisha klabu za elimu ya ushindani, ulinzi wa mlaji na udhibiti wa bidhaa bandia katika shule za msingi, sekondari na taasisi za elimu ya juu ili kujenga kizazi chenye uelewa wa masuala hayo.

Akizungumza na waandishi wa habari Juni 20, 2026, katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea jijini Dodoma, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma wa FCC, Bi. Roberta Feruzi, amesema mpango huo utatekelezwa kupitia klabu zitakazojulikana kama Ushindani School Club. 

Amesema lengo la mpango huo ni kuwafikia wanafunzi mapema na kuwajengea uelewa kuhusu ushindani, haki za mlaji na namna ya kufanya maamuzi sahihi wanaponunua bidhaa au kupata huduma.

Feruzi amesema elimu hiyo itawasaidia wananchi kutambua bidhaa bandia, kulinda soko dhidi ya udanganyifu na kuwawezesha watumiaji kuchagua bidhaa salama na zenye ubora.

Ameeleza kuwa uelewa wa masuala ya ushindani na ulinzi wa mlaji utasaidia wananchi kufanya uchaguzi bora wa bidhaa na huduma, huku sekta binafsi ikiendelea kuchangia katika uzalishaji na ukuaji wa uchumi.

Aidha, amesema utoaji wa elimu hiyo utaendelea kupitia ofisi za kanda za FCC zilizopo Mwanza, Arusha, Mbeya, Dodoma na Dar es Salaam kwa lengo la kuhakikisha wananchi katika mikoa yote ya Tanzania Bara wanapata elimu hiyo.


Top News