Mradi wa Ujenzi wa Daraja la Zege la Gagi linalojengwa Kata ya Ndembezi Manispaa ya Shinyanga kupitia Mfuko wa Dharura (CERC) limeondoa adha ya usafiri iliyokuwa inawakabili kwa muda mrefu wananchi wa Kata hiyo na maeneo ya jirani. 

Daraja hilo lenye urefu wa mita 11.2 na upana mita 8.2 linajengwa kwenye barabara ya Gagi ambalo linaunganisha Kata za Ndembezi na Ngokolo  katika Manispaa hiyo.

Akizungumza kwenye mahojiano maalum katika ziara ya kutembelea mradi huo, Diwani wa Kata ya Ndembezi na Naibu Meya wa Manispaa ya Shinyanga Mhe. Upendo John Sawa amesema kukosekana kwa daraja hilo ni kilio cha muda mrefu kwa wananchi wa Kata hiyo kutokana na ugumu wa kupita katika eneo hilo hasa kipindi cha masika kutokana na kivuko cha awali kusombwa na maji.

"kipindi cha masika akina mama walikuwa wanajifungulia hapa, wanafunzi kwenda shule mpaka wapatikane watu wa kuwavusha, wengine wanavushwa kwa pesa, Mwenyekiti wa Serikali ya mtaa na wajumbe wake walikuwa wanakaa hapa kusubiri kuwavusha watoto ilikuwa ni adha kubwa sana" .

Amesema kwa hatua iliyofikia ya ujenzi wa daraja hilo ni furaha kubwa sana kwao na kwamba kilio cha wakazi wa Butengwa kimeisha na kuongeza kuwa daraja hilo limeleta tabasamu kwa wakazi wa mtaa wa Botengwa na Kata ya Ndembezi kwa ujumla.

Naye Meneja wa Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) Mhandisi Samson Pamphili amesema kuwa wakati wa masika eneo hilo lilikuwa halipitiki kutokana na mafuriko makubwa ambayo yalisababishwa na mvua hivyo walilipa kipaumbele kwenye mipango yao kwa kujenga daraja kupitia chanzo chochote cha pesa.

Amesema wamebahatika kupata fedha za kutekeleza kazi hiyo kiasi cha shilingi 105,477,950 kupitia Mfuko wa Dharura (CERC) ambao unafadhiliwa na Benki ya Dunia na unalenga kuboresha miundombinu ya barabara iliyoharibiwa na mafuriko.  

Ameongeza kuwa muda wa ujenzi wa daraja hilo ni miezi sita na kwamba ujenzi ulianza Desemba 29, 2025 na unatarajia kukamilika Juni 28, 2026 lakini kwa mujibu wa Mhandisi Pamphili ujenzi wa daraja hilo umefanyika kwa haraka na mpaka sasa umefikia asilimia 93 na ifikapo Machi 28, 2026 daraja hilo litaanza kutumika.

Kwa upande wake Emmanuel Exavery Hanya Mkazi wa mtaa wa Botengwa amesema eneo hilo lilikuwa ni tishio  kabla ya ujenzi wa daraja hilo na kuongeza kuwa walikuwa wakipata shida kuvuka eneo hilo kipindi cha masika hasa wanafunzi kwenda shuleni, akina mama wajawazito na waliokuwa wakienda kwenye shughuli zao za kiuchumi. 

"Tunaishukuru serikali kwa usikivu wao kwa kuja kutatua changamoto iliyokuwepo kwenye eneo hili na kufikia hatua hii, hivyo changamoto kwenye eneo hili zimeisha na wananchi tunaweza kuvuka bila shida yeyote".








Na Mashaka Mhando, Dodoma


NAIBU Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma (MwanaFA), leo ameongoza ujumbe wa Wizara mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuwasilisha na kujadili majibu ya hoja za Bunge kuhusu Sheria ya Haki ya Kunufaika na Mauzo Endelevu (Resale Right) ya mwaka 2025.

Uwasilishaji huo wa leo, Machi 25, 2026, unalenga kutoa ufafanuzi wa kina juu ya kanuni na taratibu zitakazomwezesha msanii wa Tanzania kuendelea kupata mirabaha (Royalty) kila mara kazi yake inapouzwa tena sokoni na mtu mwingine baada ya mauzo ya awali.

Akizungumza mbele ya Kamati hiyo jijini Dodoma, Mhe. Mwinjuma amebainisha kuwa Wizara imefanyia kazi hoja zote zilizoibuliwa na Bunge ili kuhakikisha sheria hiyo ndogo inakuwa na tija na inatekelezeka bila vikwazo kwa wadau wa kazi za sanaa na ubunifu.

Mhe. Naibu Waziri ameeleza kuwa Wizara imefanya uchambuzi wa kina wa hoja za Bunge ili kuhakikisha sheria hiyo ndogo inakidhi vigezo vya kisheria na inatekelezeka bila kuleta urasimu kwa wadau wa sanaa na michezo.

“Tumejadili kwa kina na Kamati ya Bunge kuhusu namna bora ya kusimamia haki hizi za mauzo endelevu. Lengo la Serikali ya Awamu ya Sita ni kuhakikisha msanii ananufaika na jasho lake maisha yake yote, hata baada ya kuuza kazi yake kwa mara ya kwanza,” amesema Mhe. Mwinjuma na kuongeza,

"Tumeitikia wito wa Kamati na kuwasilisha majibu ya hoja mbalimbali kuhusiana na Resale Right. Lengo letu ni kuhakikisha msanii ananufaika na jasho lake hata baada ya kazi yake kupanda thamani huko sokoni,”

Sheria hiyo ya Resale Right ya mwaka 2025 inatajwa kuwa mkombozi wa wasanii wa michoro, sanamu na kazi nyingine za mikono, ambapo awali walikuwa wakikosa mapato pindi kazi zao zilipouzwa kwa bei kubwa na madalali au wamiliki wa maghala ya sanaa (Art Galleries).

Utekelezaji wa kanuni hizi za Resale Right unatajwa kuwa ni mapinduzi makubwa katika sekta ya utamaduni na sanaa, kwani Tanzania inakuwa miongoni mwa nchi zinazopiga hatua kubwa katika kulinda miliki bunifu kulingana na mabadiliko ya soko la kimataifa.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo imepokea majibu hayo na kutoa mapendekezo ya namna ya kuboresha zaidi mifumo ya ukusanyaji na usambazaji wa miraba hiyo ili kusiwe na mianya ya upotevu wa mapato kwa wasanii.

Wizara imesisitiza kuwa maboresho hayo yamezingatia mazingira ya sasa ya biashara ya sanaa ndani na nje ya nchi, huku yakilenga kuongeza mchango wa sekta ya utamaduni na sanaa katika Pato la Taifa (GDP).










WAZIRI wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar, ameagiza wadau wote katika masoko ya mitaji na dhamana wazingatie sheria na kanuni za masoko ya fedha huku wakiimarisha utoaji wa huduma kwa njia ya kidigitali.

Akizungumza Jumanne wakati wa sherehe ya 5 ya kuhitimisha kozi ya Cheti cha Sekta ya Dhamana na Shindano la Vyuo Vikuu na Taasisi za Elimu ya Juu, Balozi Omar alisisitiza haja ya kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu masoko ya mitaji na dhamana ili kuongeza uelewa na ushiriki.

“Nawaasa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) na wadau kuendelea kutoa elimu kwa umma ili kuongeza uelewa na ushiriki katika sekta hii,” alisema. 

Pia aliagiza CMSA kutekeleza kikamilifu majukumu yake ya kusimamia, kuratibu na kuendeleza masoko ya mitaji na dhamana ili kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa 2050.

Balozi Omar alibainisha kwamba uelewa zaidi wa masoko ya mitaji ni muhimu ili kuhamasisha ushiriki wa Watanzania, akieleza kuwa masoko haya yana nafasi muhimu katika upatikanaji wa mitaji kwa makampuni ya umma na binafsi. Hii inawawezesha wananchi kushiriki moja kwa moja katika uchumi na kuchangia kufanikisha malengo ya Dira ya 2050.

Aliongeza kuwa, kama ilivyo kwa sekta nyingine, masoko ya mitaji na dhamana yanahitaji wataalamu wenye ujuzi na weledi wa kutosha ili kuwezesha upatikanaji wa mitaji ya muda mrefu kwa maendeleo ya uchumi wa kisasa. Alisema kuwa hadi Desemba mwaka jana, jumla ya thamani ya uwekezaji katika masoko ya mitaji ilifikia shilingi trilioni 63.15.

Awali, Mwenyekiti wa Bodi ya CMSA, Lucas Mwimo, alishukuru serikali kwa kuweka mazingira bora yanayowezesha mamlaka kukuza sekta ya masoko ya mitaji. Bw Mwimo alibainisha jitihada za CMSA kutoa mafunzo, kuanzisha bidhaa bunifu, na kuhamasisha ushiriki wa soko wa ndani na nje ya nchi.

Mkurugenzi Mtendaji wa CMSA, CPA. Nicodemus Mkama, alibainisha kuwa wahitimu wa kozi hiyo wanakidhi viwango vya kimataifa, na hivyo kuimarisha ujuzi wa wataalamu wanaotoa huduma katika masoko ya mitaji. “Kuhakikisha tunatoa elimu bora na kujenga uwezo wa wataalamu kunalingana na utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050, inayolenga kuendeleza wataalamu wenye weledi,” alisema.

CMSA pia ilianzisha Shindano la Vyuo Vikuu la Masoko ya Mitaji, lililoshirikisha wanafunzi kote nchini kupitia maswali ya mtandaoni. Jumla ya wanafunzi 28,383 walishiriki, ikizidi malengo kwa zaidi ya asilimia 140. Washindi watano wa juu walipatiwa zawadi za fedha kuanzia shilingi milioni 3 hadi 700,000, na pia watapata mafunzo nchini Nigeria pamoja na kutembelea makampuni makubwa yanayojihusisha na masoko ya mitaji.

Ili kuongeza idadi ya wataalamu waliokidhi viwango vya kimataifa, CMSA inashirikiana na Chartered Institute for Securities & Investment (CISI).

Akizungumza, Naibu Gavana  wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Yamungu Kayandabila, alisisitiza umuhimu wa ujumuishaji wa kifedha na elimu ya kifedha. “Mitandao ya kidigitali imebadilisha mfumo wa kifedha, ikiruhusu elimu ya kifedha mtandaoni. Kufunga pengo la kifedha kidijitali kati ya vijijini na mijini ni jambo kuu katika sera yetu ya fedha na mfumo wa kitaifa wa ubunifu wa kifedha,” alisema.




Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo imepitisha randama ya mpango na makadirio ya bajeti ya matumizi ya kawaida pamoja na mpango wa maendeleo kwa mwaka wa fedha 2026/2027 wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. 

Mpango huo umepitishwa na kamati Machi 24, 2026 chini ya Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Husna Sekiboko,  ambae amesema mpango huu unakwenda  kuwa chachu ya kuandaa vijana wenye ujuzi.

Mhe. Sekiboko amesisitiza kuhakikisha mtiririko wa fedha utakaowezesha miradi yote ya maendeleo inatekelezwa na kukamilika kwa wakati. 

" kwakweli tumeshuhudia  miradi mingi mikubwa mizuri ambayo inajenga imani ya wananchi kwa Serikali na kuongeza tija katika maendeleo," amesema Mhe Sekiboko

Pia ameiomba Wizara kushirikiana kwa Karibu na Wizara ya Fedha kuhakikisha fedha za miradi ya maendeleo kwa sekta ya elimu zinatolewa kwa wakati. Na kwa mtiririko unaowezesha utekelezaji wenye ufanisi.

Kwa upande wake, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, amewashukuru wajumbe wa Kamati hiyo kwa kupokea na kupitisha randama ya bajeti ya wizara na kuahidi kuwa wizara itaendelea kuboresha mifumo na mazingira ya utoaji elimu  ili kuhakikisha kila mtoto wa Kitanzania anapata elimu na ujuzi kwa usawa na ujumuishi.















Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imesisitiza kuimarishwa kwa ushirikiano kati ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na Chuo Kikuu cha Vienna  katika nyanja za sayansi na teknolojia, ikiwemo nishati ya jua, ili kuzalisha wataalamu wenye ujuzi kwa manufaa ya pande zote mbili.

Hayo yameelezwa na Naibu Makamu Mkuu wa Chuo (Taaluma) kutoka UDSM, Prof. Rose Upor alipofanya mazungumzo na  Ujumbe wa Austria ulioongozwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje anayeshughulikia masuala ya kisiasa, Mhe. Balozi Dkt. Hannah Liko, ulipotembelea chuoni hapo  Machi 24, 2026 kwa lengo la kuimarisha ushirikiano katika sekta ya elimu kati ya Tanzania na Austria.

Prof. Upor amesema ili kuimarisha zaidi ushirikiano uliopo kati ya UDSM  na Chuo Kikuu cha Vienna, kuna umuhimu wa kuongeza ufadhili wa masomo katika kada mbalimbali pamoja na kubadilishana wataalamu watakaoweza kufundisha hata kwa njia ya mtandao. 

Naye Balozi na Mwakilishi wa Kudumu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mjini Vienna, Balozi Naimi S.H. Aziz, amesema kuwa ushirikiano kati ya Tanzania na Austria katika sekta ya elimu una mchango mkubwa katika kukuza ujuzi, kuimarisha taasisi na kuongeza ubora wa huduma nchini.

Kwa upande wake, Dkt. Liko amepongeza ushirikiano uliopo kati ya UDSM na Chuo Kikuu cha Vienna, huku akipendekeza kuanzishwa kwa mafunzo ya lugha ya Kijerumani katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Amesema kuwa kuimarika kwa ushirikiano katika sekta ya elimu kutachangia maendeleo ya kiuchumi na kidiplomasia kwa mataifa yote mawili.

Ushirikiano kati ya UDSM na Chuo Kikuu cha Vienna unalenga maeneo manne makuu ya kimkakati, yakiwemo ubadilishanaji wa wanafunzi ili kuwapatia uzoefu wa kimataifa, ubadilishanaji wa wafanyakazi wa kitaaluma na kiutawala, utekelezaji wa tafiti za pamoja zinazogusa changamoto za kimataifa kama utawala bora na maendeleo endelevu, pamoja na uchapishaji wa kazi za pamoja za kitaaluma ili kuhakikisha mitazamo ya Afrika inawakilishwa vyema kimataifa.
















Top News