WANANCHI wa kijiji cha Ng'ongo kata ya Mtowisa wilayani Sumbawanga wameiomba serikali kuwajengea nyumba watumishi wa Afya na kuongeza wahudumu katika Zahanati ya kijiji hicho huku Zahanati hiyo ikiwa na wahudumu wawili wote wakiwa ni wauguzi hali inayohatarisha Afya za wakazi wa eneo hilo.

Akijibu ombi hilo kwa wananchi Waziri wa katiba na sheria Juma Homera aliwahakikishia wakazi wa eneo hilo kuwa changamoto hiyo itakwenda kutatuliwa kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo pamoja na wananchi huku waziri huyo akichangia mifuko 100 ya saruji ili kuanza kwa ujenzi wa nyumba ya watumishi wa Afya na kuimarisha huduma za matibabu katika Zahanati hiyo.

Waziri wa katiba na sheria Juma Homera amefungua Zahanati ya kijiji cha Ng'ongo iliyogharim Milioni 120 ikiwa Zahanati hiyo ilianza kujengwa kwa nguvu za wananchi kwa milioni 20 huku serikali ikikamilisha ujenzi huo kwa sh. milioni 100.





Jane Mwakyoma - Rukwa.

SERIKALI Imewaomba wakulima mkoani Rukwa kuwa na subra ya upandaji wa bei ya mahindi  wakati serikali inapolifanyia kazi suala la bei za mahindi nchini.

Akitoa ufafanuzi huo baada ya mkuu wa wilaya ya Sumbawanga akimwakilisha mkuu wa mkoa wa Rukwa Nyakia Chirukile baada ya kumuomba Waziri wa katiba na sheria kuhusu serikali kupandisha bei ya mahindi mkoani humo baada ya kukagua ujenzi wa stendi ya mabasi Laela.

Homera amesema serikali ya Dk. Samia Suluhu Hassan inashughulikia changamoto za wananchi katika kuhakikisha wananchi wake wanaondokana na changamoto ya bei ndogo ya mahindi ili kuwainua wakulima kiuchumi.

" Niseme suala la bei ya mazao kila sehemu hii changamoto ipo, ukienda mimi jimbo langu ni Namtumbo, pale wanalima mahindi miongoni mwa mikoa inayolima mahindi ni Ruvuma ,Rukwa, Katavi nadhani na Iringa pia lakini bei ya mahindi huku kwetu imeshuka kwa kiwango kikubwa lakini ndugu zangu niwatoe mashaka hili jambo serikali ya CCM inayoongozwa na Dk. Samia Suluhu Hassan chini ya waziri wa kilimo Daniel Chongoro, inalifahamu kwaiyo tuendelee kuwa na subra kidogo serikali inapolifanyia kazi " amesema Homera.

Pia Homera amesema suala la mbolea serikali ya awamu ya sita inalishughulikia suala hilo na kuwataka wananchi kuendelea kusubili huku serikali ikisisitiza wakulima kuendelea kujiandikisha ili kupata mbolea za ruzuku.

Aidha amewataka wananchi kutoa ushirikiano kwa vyombo vya sheria kwa watu wanaotaka kuvuruga amani katika nchi.

Pia amesema wananchi wasikubali kudanganywa kwasababu ya maslahi ya watu wachache na badala yake wahakikishe wanailinda amani ya nchi kwa wivu mkubwa ili kuendelea na shughuli zao za kiuchumi kwa amani na utulivu.

Waziri wa katiba na sheria Juma Homera yupo mkoani Rukwa kwa ziara ya siku nne kwa lengo la kukagua, kutembelea,kuweka mawe ya msingi,kufungua miradi ya maendeleo na kusikiliza kero za wananchi.



Jane Mwakyoma,Rukwa.

WAZIRI wa katiba na sheria Juma Homera ameagiza Taasisi ya kupambana na rushwa (TAKUKURU) mkoani Rukwa kuchunguza madai ya wahudumu wa Afya wa hospital ya wilaya Mtowisa wilayani Sumbawanga wakidaiwa kuwatoza wananchi shilingi 40,000 kwa watoto chini ya miaka mitano wanapopatiwa matibabu na waliojifungua watoto wa kiume hutozwa shilingi elfu kumi ikiwa ni kinyume cha sheria na matakwa ya serikali.

Akitoa maagizo hayo mara baada ya wananchi kutoa kero zao katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika kijiji cha Mtowisa kata ya Mtowisa wilayani Sumbawanga Homera alisema serikali imeweka mipango ya wajawazito na watoto chini ya miaka mitano kutibiwa bure katika hospitali za serikali na kuwa endapo kutakuwa na wahudumu wa Afya watakao kwenda kinyume na mtakwa ya serikali watachukuliwa hatua za kisheria na kinidhamu.

"Kwanza inasikitisha sana huwezi kuwatoza pesa wamama wajawazito akijfungua mtoto wa kiume unamtoza pesa, akijfungua mtoto wa kike unamtoza pesa,jambo hili Taasisi ya kupambana na rushwa waanze kufanyia kazi mara moja ikiwemo na kufanya uchunguzi kwa kina katika hospitali ya wilaya na kuanza kuwabaini wahudumu wa Afya ambao siyo wema kwa watanzania tukianza kuyafumbia macho haya kesho wataiba hadi watoto watawapa watoto watu wengine."

"Sasa lazima tuhakikishe kwamba kama mtu atatozwa sh.10000 lazima mtumishi huyo achukuliwe hatua ,ofisi ya mkuu wa wilaya mpo hapa na TAKUKURU hakikisheni tarehe ya kufanya majumuisho tupate na kama mmetoa katazo tupate taarifa hiyo "amesisitiza Homera.

Aidha amepiga marufuku kwa watumishi wa Afya kuwatoza fedha wamama wajawazito na watoto chini ya miaka mitano kuwa serikali ya awamu ya sita imeagiza kundi hilo kutibiwa bure katika hospitali za serikali.

"kwanza Ni marufuku kuwatoza wananchi fedha sh.40000 au elifu kumi, serikali imeagiza wamama wajawazito na watoto chini ya miaka mitano kutibiwa bure,kuna baadhi ya watumishi wasiyo waadilifu wanaichonganisha serikali na wananchi hatutakubali mtumishi atuchonganishe" alisisitiza Homera.

Aidha amewataka viongozi wa sekta mbalimbli nchini kujijengea mazoea ya kusikiliza kero na changamoto za wananchi na kuzitatua ili wananchi waendelee kuwa na imani na serikali yao.

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Sumbawanga Nyakia Chirukile amekili kuwepo kwa changamoto ya wajawazito wakati wa kujifungua na watoto chini ya miaka mitano kutibiwa kwa kutozwa fedha ikiwa ni kinyume na taratibu zilizowekwa.

Amesema alipigiwa simu na baadhi ya wananchi kueleza kero hiyo ambapo alimwagiza mganga mkuu wa wilaya kulifanyia kazi suala hilo ikiwemo kupatikana kwa kipimo cha tyaphodi ambacho mpaka sasa hospitali hiyo haina kipimo hicho na kuwa wananchi wamekuwa wakielekezwa kutozwa kiasi kikubwa cha pesa wakidai kipimo kilichopo siyo mali ya serikali bali ni mali ya mtu binafsi.





Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Mauritius, Kamishna wa Polisi (CP) Suzan Kaganda, mwenye makazi yake ya kikazi Jijini Harare, Zimbabwe, amewasilisha Hati za Utambulisho kwa Rais wa Jamhuri ya Mauritius, Mhe. Dharambeer Gokhool, katika hafla iliyofanyika Julai 6, 2026, Ikulu ya Serikali iliyopo Reduit, Mauritius.

Baada ya kuwasilisha hati hizo, Balozi Kaganda alifanya mazungumzo na Mheshimiwa Rais Gokhool, ambaye alimpongeza kwa uteuzi wake na kumkaribisha rasmi katika eneo lake la uwakilishi, huku Rais huyo pia akimhakikishia ushirikiano na Serikali ya Mauritius katika kipindi chote cha utekelezaji wa majukumu yake ya kidiplomasia.

Kwa upande wake, Balozi Kaganda alishukuru kwa mapokezi mazuri aliyopatiwa na kuahidi kuendeleza ushirikiano wa karibu na Serikali ya Mauritius katika kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Mauritius ambapo aliweka wazi kuwa dhamira yake ni kuendeleza ushirikiano katika sekta za biashara, uwekezaji, utalii na Uchumi wa Buluu kwa manufaa ya wananchi na maendeleo ya nchi hizo mbili.

Balozi (CP) Kaganda pia anaiwakilisha Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Zimbabwe, akiwa na makazi ya kikazi jijini Harare.






📍NIRC: DODOMA

Tume ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC) imeanza kuweka mikakati ya jinsi ya kusafirisha mitambo yake mikubwa ya kuchimba visima virefu kwenda maeneo mbalimbali nchini, hususani yale yenye changamoto kubwa ya upatikanaji wa maji chini ya ardhi, mara baada ya kukamilisha kazi katika shamba la Chinangali.

Mkurugenzi Mkuu wa NIRC, Raymond Mndolwa, ametoa agizo hilo kwa Idara ya Mitambo, ya Tume hiyo kutathmini namna bora ya kusafirisha mitambo hiyo bila kuathiri miundombinu ya barabara kutokana na uzito wake mkubwa.

“Tuone namna bora kwa Idara husika kushauri kama tunaweza kusafirisha mitambo hii nusu nusu (kwa kuifungua) kutokana na uzito wake, ili isiathiri barabara zetu inapokwenda mikoa tofauti,” amesisitiza Mndolwa.

Agizo hilo amelitoa wakati wa ziara yake katika shamba la vijana la mradi wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) lililopo Chinangali mkoani Dodoma.

Ziara hiyo ililenga kukagua maendeleo ya ujenzi wa barabara za ndani, mabwawa,uchimbaji wa visima na uwekaji wa miundombinu ya Umwagiliaji katika mashamba hayo,inayotekelezwa na Tume hiyo.

Katika ziara hiyo, Mndolwa alikagua mtambo huo wa kisasa wenye uwezo wa kuchimba visima virefu hadi mita 1,800 chini ya ardhi, ambao kwa sasa upo Chinangali kwa ajili ya kuchimba visima viwili vya mwisho. Visima hivyo vitakamilisha jumla ya visima 40 vinavyochimbwa na NIRC shambani hapo, sambamba na mabwawa matatu ambapo mawili tayari yamekamilika ili kuongeza kasi ya upatikanaji wa maji.

Mndolwa aliambata na wataalamu mbalimbali akiwemo Mkurugenzi wa Idara ya Uendelezaji Miundombinu Mhandisi Leopard Runji, Mhandisi wa Mkoa wa Dodoma Oswald Urassa na Muendesha Mitambo hiyo ya Visima virefu Mosses Mkude. 







Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) umeendelea kuimarisha juhudi za kupanua wigo wa hifadhi ya jamii nchini kwa kuwahamasisha wananchi waliojiajiri kujiunga na Hifadhi Skimu, huku ukiwahimiza waajiri wenye malimbikizo ya michango kunufaika na msamaha wa tozo uliotolewa na Mfuko. Wito huo umetolewa wakati wa Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba).

Akizungumza baada ya kutembelea banda la NSSF katika maonesho hayo, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Bw. Masha Mshomba, alisema ameridhishwa na mwitikio wa wananchi pamoja na huduma zinazotolewa na Mfuko, hususan elimu kuhusu hifadhi ya jamii, usajili wa wanachama wapya na huduma za kidijitali.

Bw. Mshomba alisema banda la NSSF limeendelea kuwa jukwaa muhimu la kutoa elimu kwa wananchi kuhusu nafasi ya hifadhi ya jamii katika kuboresha ustawi wa maisha, kupunguza umaskini, kuimarisha nguvu kazi na kuongeza uzalishaji katika uchumi wa taifa.

Kupitia Hifadhi Skimu, alisema wananchi waliojiajiri wanaweza kujiunga na NSSF kwa hiari na kuchangia kwa viwango vinavyolingana na uwezo wao.

Alieleza kuwa kiwango cha chini ni shilingi 30,000 kwa mwezi kinachomwezesha mwanachama kupata huduma za matibabu, huku mchango wa shilingi 52,200 ukimpa mwanachama huduma za matibabu yeye mwenyewe, mwenza wake na watoto wasiozidi wanne.

Alifafanua kuwa wanachama wa skimu hiyo pia hunufaika na mafao ya uzazi, ulemavu, pensheni ya uzee na urithi, akibainisha kuwa mfumo huo unaruhusu michango kufanyika hata kila siku ilimradi ifikie kiwango cha mwezi.

Bw. Mshomba alisema mafanikio hayo yametokana na maboresho ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambayo yameongeza ushiriki wa wananchi waliojiajiri katika mfumo rasmi wa hifadhi ya jamii.

Katika huduma za kidijitali, alisema NSSF imeboresha mifumo yake inayowezesha wanachama na waajiri kujihudumia popote kupitia NSSF Portal bila kufika ofisini, hatua iliyorahisisha upatikanaji wa huduma kwa wakati.

Katika hatua nyingine, Bw. Mshomba alisema NSSF imetoa msamaha wa tozo kwa waajiri wenye madeni ya michango kuanzia Juni hadi Desemba 2026, ili kuwapa fursa ya kulipa madeni ya msingi na kupunguza mzigo wa tozo.

Alisema waajiri watakaolipa madeni yao ya msingi kuanzia Juni hadi Agosti 31, 2026 watanufaika na msamaha wa asilimia 100 ya tozo, mradi waendelee kulipa michango ya sasa kwa wakati hadi Januari 2027. Wataakaoanza kulipa kati ya Septemba 1 na Oktoba 31 watanufaika na msamaha wa asilimia 75, huku watakaoanza kulipa kati ya Novemba 1 na Desemba 31 wakinufaika na msamaha wa asilimia 50.

Aliwataka waajiri kutumia fursa hiyo kuongeza tija katika uzalishaji badala ya kuelekeza rasilimali katika kulipa tozo, huku akisisitiza umuhimu wa kuwasilisha michango kwa wakati ili kulinda haki za wafanyakazi.

Pia aliwahimiza waajiriwa kufuatilia michango yao na kutoa taarifa NSSF endapo michango yao haiwasilishwi kwa mujibu wa sheria.

Akizungumzia ukuaji wa Mfuko, Bw. Mshomba alisema thamani ya NSSF imeongezeka kutoka shilingi trilioni 4.8 mwezi Machi 2021 hadi shilingi trilioni 9.8 kufikia Juni 30, 2026 kwa mujibu wa hesabu zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), huku hesabu ambazo bado hazijakaguliwa katika mwaka wa fedha ulioishia Juni 30, 2026, zikionesha thamani ya zaidi ya shilingi trilioni 11.6.

Alieleza kuwa ukuaji huo umetokana na ongezeko la michango, uwekezaji wenye tija pamoja na matumizi ya teknolojia katika utoaji wa huduma.

Kwa upande wa uwekezaji, alisema NSSF imeanza kuwekeza nje ya nchi baada ya kupata kibali kutoka Benki Kuu ya Tanzania (BoT), ikilenga masoko ya mitaji na miradi ya majengo ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), ikiwemo ujenzi wa majengo ya biashara jijini Nairobi, Kenya, yatakayoongeza mapato na kuimarisha uwezo wa Mfuko.









Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mhe. Dkt. Rhimo Nyansaho, amewapongeza viongozi wa  Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kwa juhudi wanazozifanya za kuimarisha ulinzi na usalama nchini.

Amesema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari kwenye maadhimisho ya miaka 50 ya biashara ya kimataifa jijini Dar es Salaam  Sabasaba, Julai 6, 2026, amesisitiza kuwa vyombo hivyo vya ulinzi vimekuwa vikiendelea kulinda amani ya nchi, jambo linalowezesha wananchi kufanya shughuli za maendeleo na kufanikisha utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya 2050.

Aidha amesema shirika  la JKT linafanya kazi za uzalishaji mali pamoja na kuwafundisha vijana, hatua inayosaidia kuwaandaa kujitegemea na kujiajiri.

Ameeleza kuwa kupitia maonesho hayo, taasisi hizo zimepata nafasi ya kuonesha shughuli mbalimbali zinazofanyika kwenye vikosi vyao, ikiwemo kutoa huduma kwa wananchi na mafunzo kwa vijana.

Amesema kampuni ya usafi na unyunyuzi dawa ya SUMA JKT ambayo imefanikiwa kuajiri vijana 4,800, hatua inayoonesha mchango wa taasisi hizo katika kupunguza changamoto ya ajira nchini.



Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Ubongo (MOI) imesema itaendelea kuimarisha tafiti zinazolenga kuzalisha afua za matibabu zinazozingatia mazingira na vinasaba vya Watanzania, ili kuboresha huduma za matibabu ya magonjwa ya mifupa na mfumo wa fahamu.

Akizungumza na waandishi wa habari Mkurugenzi Mtendaji wa MOI, Balozi Dkt. Mpoki Ulisubisya, Jijini Dar es Salaam Julai 6, 2026, kwenye Maadhimisho ya Miaka 50 ya Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba).

Amesema mara nyingi tiba zinazotumika hutokana na matokeo ya tafiti zilizofanyika katika nchi zilizoendelea pamoja na baadhi ya nchi za bara la Afrika, ambapo afua hizo zinaweza kuwa zimezingatia watu wenye vinasaba tofauti, hivyo wao wameona umuhimu wa kufanya tafiti zitakazozalisha afua zinazokidhi mazingira ya Tanzania.

Aidha, amesema MOI imetimiza miaka 30 tangu kuanzishwa kwake na imeendelea kujikita katika maeneo makuu matatu ambayo ni kutoa huduma kwa wagonjwa wa mifumo ya ubongo na mifupa, kufundisha huduma hizo kwa wananchi na wataalam katika ngazi ya shahada ya kwanza, shahada ya pili na ubobezi, pamoja na kufanya tafiti.

Pia amesema taasisi hiyo imeweza kutoa mafunzo kwa wananchi na wataalam kutoka ndani na nje ya Tanzania, hususan katika ukanda wa Afrika Mashariki, Kati, Kusini na Magharibi, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha huduma za afya katika kanda hiyo.





📍Dar es Salaam

Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Dkt. Janet Lekashingo, amesema Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 imeipa sekta ya madini nafasi ya kimkakati ya kuongoza mageuzi ya uchumi wa Tanzania kupitia uongezaji thamani wa madini, ushirikishwaji wa watanzania na matumizi ya teknolojia za kisasa katika shughuli za uchimbaji wa madini.

Akizungumza mapema leo Julai 6, 2026, alipotembelea mabanda ya taasisi zilizo chini ya Wizara ya Madini katika Kijiji cha Madini kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), Dkt. Lekashingo amesema Tume ya Madini imejipanga kikamilifu kutekeleza malengo ya Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 ili sekta ya madini iwe nguzo muhimu ya ukuaji wa uchumi na maendeleo endelevu.

Amesema utekelezaji wa dira hiyo unalenga kuongeza thamani ya madini ndani ya nchi badala ya kuyasafirisha ghafi, kuimarisha utafiti wa jiolojia ili kubaini maeneo mapya yenye rasilimali za madini, kuongeza ushiriki wa watanzania katika miradi ya uchimbaji wa madini pamoja na kuhamasisha matumizi ya teknolojia rafiki kwa mazingira na zinazoongeza usalama migodini.

Aidha, amewataka wananchi kutembelea banda la Tume ya Madini ili kupata elimu kuhusu huduma zinazotolewa na Tume pamoja na fursa zilizopo katika mnyororo wa thamani wa madini, ikiwemo taratibu za kushiriki biashara ya madini na kuuza madini kupitia masoko na vituo vya ununuzi wa madini.

Katika hatua nyingine, Dkt. Lekashingo amewapongeza viongozi na watumishi wa Tume ya Madini kwa kuvuka lengo la ukusanyaji wa mapato katika mwaka wa fedha 2025/2026, akisema mafanikio hayo yanadhihirisha uwajibikaji na usimamizi madhubuti wa sekta ya madini.

“Mmetuheshimisha kwa kuvuka lengo la ukusanyaji wa mapato, lakini tusibweteke. Bado tuna wajibu mkubwa wa kuhakikisha tunavuka lengo la kukusanya shilingi trilioni 1.4 katika mwaka wa fedha 2026/2027,” amesema.

Wakati huohuo, Dkt. Lekashingo ametembelea mabanda mbalimbali ya taasisi zilizo chini ya Wizara ya Madini, ikiwemo Tume ya Madini, Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST), Kituo cha Jemolojia Tanzania (TGC) na Wadau wa Madini kabla ya kutembelea mabanda ya Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Banda la Zanzibar na Wizara ya Nishati.

Akiwa katika banda la Wizara ya Nishati, Dkt. Lekashingo ameiomba Wizara hiyo kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kuhakikisha umeme unafikishwa katika maeneo yote yenye shughuli za uchimbaji na uchenjuaji wa madini nchini ili kuongeza tija kwa wachimbaji, kuimarisha uzalishaji, kuongeza thamani ya madini na kuendeleza mchango wa sekta ya madini katika ukuaji wa uchumi na Pato la Taifa.












Top News