Na Oscar Assenga, TANGA

KATIBU Tawala wa Mkoa wa Tanga Rashid Mchatta amefungua kikao kazi cha Wakurugenzi na Mameneja wa Huduma kwa Wateja wa Mamlaka za Maji nchini huku akisisitiza matumizi teknolojia ya kisasa katika kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi ili kuongeza ufanisi katika utendaji wao.

Wito huo umetolewa jijini Tanga na Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga, Rashid Mchatta, aliyemwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, wakati akifungua kikao kazi cha Wakurugenzi wa Huduma kwa Wateja wa Sekta ya Maji nchini.

Kikao hicho kinafanyika chini ya kaulimbiu “Huduma Janja: Matumizi ya Teknolojia kwa Huduma Bora kwa Wateja”, kikilenga kuwawezesha wakurugenzi na mameneja hao kubadilishana uzoefu na kujadili mbinu mbalimbali za kuboresha huduma kwa wananchi.

Mchatta aliipongeza Serikali inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuiamini na kuiwezesha Wizara ya Maji kutekeleza miradi na programu mbalimbali zinazolenga kuboresha upatikanaji wa maji safi na huduma za usafi wa mazingira nchini.

Pia aliipongeza uongozi wa Wizara ya Maji unaoongozwa na Waziri wa Maji, Jumaa Aweso, Naibu Waziri, Mhandisi Mathew Kundo, Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu, Rose Ambrose, kwa juhudi wanazofanya katika kusimamia utekelezaji wa majukumu ya wizara hiyo.

Alisema mafanikio yanayoonekana katika sekta ya maji, kuanzia utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati hadi uboreshaji wa huduma kwa wananchi, yanaonesha kuwa uongozi wa wizara hiyo umejikita katika kuhakikisha huduma zinaboreshwa kila siku.

“Viongozi hawa wameonesha weledi, uzoefu na uthubutu katika kusimamia sekta ya maji. Ushirikiano wao umeendelea kuleta mafanikio yanayoonekana na wananchi wanaendelea kushuhudia mabadiliko katika huduma za maji na usafi wa mazingira,” alisema Mchatta.

Alisema kikao hicho ni fursa muhimu kwa wakurugenzi na mameneja wa huduma kwa wateja kujifunza, kubadilishana uzoefu na kutafuta suluhisho la changamoto zinazojitokeza katika utoaji wa huduma.

Kwa mujibu wa Mchatta, mafunzo hayo pia yanahusu ufanisi wa biashara katika mamlaka za maji pamoja na mbinu za uwekezaji binafsi, ambapo wataalamu kutoka UTT-AMIS wanashiriki kutoa elimu kwa washiriki.

Aliwataka washiriki kutumia kikamilifu fursa hiyo kujifunza mbinu mpya, kubadilishana uzoefu na kujadili changamoto zinazowakabili katika utoaji wa huduma kwa wateja.

“Ninaamini mafunzo haya yatakuwa chachu ya kuboresha ufanisi mtakaporudi katika vituo vyenu vya kazi na hivyo kuongeza ubora wa huduma mnazozitoa kwa wananchi,” alisema.

JUKWAA LA WAKURUGENZI LAZIDI KUKUA

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Wakurugenzi wa Huduma kwa Wateja wa Mamlaka za Maji nchini, Alawi Ahmad, alisema jukwaa hilo ni sehemu muhimu ya uongozi katika sekta ya maji, kwa kuwa linawapa nafasi wakurugenzi na mameneja kukutana, kujadiliana na kutafuta suluhisho la changamoto zinazowakabili katika utoaji wa huduma.

Alisema jukwaa hilo limekuwa likifanya vikao kila mwaka na kwa sasa lina takribani miaka 10 tangu kuanzishwa kwake.

“Jukwaa hili limekuwa likitusaidia kutatua changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika utoaji wa huduma kwa wateja na pia limetumika kama sauti ya pamoja ya wakurugenzi wa huduma kwa wateja katika sekta ya maji,” alisema Ahmad.

Naye Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mhandisi  Abbas Muslim Pyarali  alisema kikao hicho kinawakutanisha wakurugenzi wa mamlaka za maji wanaojikita katika utoaji wa huduma kwa wateja.

Abbas ambaye ni Mkurugenzi Msaidizi wa Usafi wa Mazingira kutoka Wizara ya Maji alisema kikao hicho kitakachodumu kwa siku tatu kitawapa washiriki nafasi ya kupata mafunzo maalumu na kubadilishana uzoefu kuhusu namna bora ya utoaji wa huduma kwa wananchi.

Alisema hatua hiyo ni sehemu ya juhudi za Wizara ya Maji za kuhakikisha huduma za maji safi na usafi wa mazingira zinaendelea kuboreshwa nchini.







Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mheshimiwa Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.), amekutana na kuagana na Balozi wa Umoja wa Ulaya nchini Christine Grau, kufuatia kukamilika kwa muda wake wa uwakilishi nchini.

Katika mazungumzo yao, Mheshimiwa Waziri Kombo alimpongeza Balozi Grau kwa mchango wake katika kuendeleza mahusiano kati ya Tanzania na Umoja wa Ulaya, hususan katika maeneo ya ushirikiano wa maendeleo, biashara na uwekezaji, Global Gateway, sekta binafsi, pamoja na majadiliano ya wazi kati ya pande hizo mbili.

Ameelezea azma ya Tanzania kuendelea kushirikiana na Umoja wa Ulaya katika misingi ya kuheshimiana, uwazi na manufaa ya pande zote, huku akimtakia Balozi Grau kila la kheri katika majukumu yake yajayo.

Kwa upande wake, Balozi Grau aliishukuru Serikali ya Tanzania kwa ushirikiano alioupata katika kipindi cha uwakilishi wake nchini, na kusisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano wa kimkakati kupitia majadiliano ya wazi na ushirikiano wa katika sekta muhimu maendeleo, kati ya Tanzania na Umoja wa Ulaya.
















MWENYEKITI wa Jumuiya ya Wazazi ya chama cha mapinduzi (CCM) Wilaya ya Siha, mkoani Kilimanjaro, Mwalimu Meijo Laizer, amempongeza Mkuu wa Mkoa wa zamani, Aggrey Mwanri kufuatia uteuzi wake, wa Naibu katibu mkuu wa chama hicho Bara.

Amesema   uongozi wa kweli haupatikani kwa bahati bali hujengwa kupitia uaminifu, nidhamu, uvumilivu na utumishi wa muda mrefu.

Laizer ametoa pongezi hizo kupitia ujumbe alioupa jina la "Kalamu ya Maridhiano", akieleza kuwa, uteuzi wa Mwanri unadhihirisha kuwa kazi njema na rekodi bora za utumishi huzungumza kwa nguvu kuliko maneno akisema hakuna anayeweza kuzuia Mungu kumuinua mtu aliyeandaliwa kwa wakati wake.

Amesema historia huandikwa na viongozi wanaotumikia kwa uadilifu na si kwa makelele, akisisitiza kuwa Mwanri ameandika ukurasa mpya wa heshima ndani ya CCM kutokana na utendaji wake.

Ameongeza kuwa cheo kinaweza kutolewa kwa kalamu, lakini heshima ya uongozi hujengwa kwa matendo, ndiyo maana uteuzi wake umepokelewa kwa furaha na heshima kubwa.

Laizer amesema CCM imeendelea kuthibitisha kuwa huwatambua viongozi wanaoweka mbele maslahi ya Chama na Taifa, akibainisha kuwa Siha imeendelea kuwa eneo linalozalisha viongozi wenye busara, hekima na uzalendo. 

Aidha amesema mafanikio ya Mwanri ni motisha kwa vijana na ushahidi kwamba uaminifu, kujituma na nidhamu bado vina thamani katika uongozi.

Akihitimisha ujumbe wake, Laizer amemtakia Mwanri mafanikio katika majukumu yake mapya na kumtaka aendelee kuwa mfano wa uongozi bora.

 "Hongera Mheshimiwa Aggrey Mwanri. Endelea kuwa taa ya uongozi, nguzo ya Chama na mfano wa uzalendo kwa vizazi vijavyo. Songa mbele kwa ujasiri mkubwa."amesema Laizer.



Na Janeth Raphael - MichuziTv .

WAKATI Tanzania ikiendelea kupanua sekta ya usafiri wa anga kupitia ongezeko la ndege mpya, Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) kimesema kinaandaa mazungumzo na Serikali ili kuwezesha wanafunzi wanaosomea urubani pamoja na kozi nyingine za anga kupata mikopo ya elimu, hatua inayolenga kuongeza idadi ya wataalamu wa ndani na kupunguza utegemezi wa wataalamu kutoka nje ya nchi.

Mkuu wa NIT, Dkt. Prosper Mgaya, amesema gharama za mafunzo ya urubani na taaluma nyingine za anga bado ni kubwa kwa Watanzania wengi, jambo linalowazuia vijana wenye sifa na uwezo kujiunga na masomo hayo. Amesema upatikanaji wa mikopo utatoa nafasi kwa vijana wengi zaidi kufikia ndoto zao na kuchangia maendeleo ya sekta hiyo.

Kwa mujibu wa Dkt. Mgaya, tafiti zilizofanywa kwa kushirikiana na Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) zimeonyesha kuwa Tanzania bado ina upungufu mkubwa wa marubani, hali inayolazimisha waajiri kutegemea wataalamu kutoka nje ya nchi.

Amesema NIT imejipanga kuwa sehemu ya suluhisho kwa kuongeza uwezo wa kuzalisha wataalamu wa anga watakaokidhi mahitaji ya soko la ajira linaloendelea kukua.

"Mahitaji ya marubani yanaongezeka kadri sekta ya anga inavyopanuka. Lengo letu ni kuhakikisha Watanzania wanapata nafasi ya kusomea taaluma hizi bila kuzuiwa na gharama kubwa za mafunzo," alisema Dkt. Mgaya.

Amefafanua kuwa uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali katika sekta ya usafiri wa anga, ikiwemo ununuzi wa ndege 16 za kisasa, umeongeza hitaji la marubani na wataalamu wengine wa anga wenye ujuzi wa hali ya juu.

Amesema ndege hizo zinahitaji kuendeshwa na wataalamu wa kutosha kila wakati, hivyo bila kuongeza idadi ya marubani wa ndani, taasisi kama ATCL zitaendelea kutegemea wataalamu kutoka nje, jambo linaloongeza gharama za uendeshaji.

Kutokana na hali hiyo, NIT inatarajia kuwasilisha hoja kwa Serikali ili wanafunzi wanaosomea urubani na fani nyingine za anga wanufaike na mfumo wa mikopo ya elimu, hatua itakayopanua fursa za masomo na kuongeza idadi ya wataalamu wa Kitanzania katika sekta hiyo.

Mbali na mpango huo, Dkt. Mgaya alisema chuo hicho kimeendelea kuboresha mazingira ya kujifunzia na kupunguza ada katika baadhi ya kozi kwa takribani asilimia 50, huku kikiongeza uwekezaji katika vifaa na ubora wa mafunzo.

Amebainisha kuwa NIT tayari imezalisha wataalamu wengi katika sekta ya usafirishaji, wakiwemo zaidi ya wahandisi na mafundi wa ndege 100 pamoja na wahudumu wa ndege zaidi ya 23, ambao wanaendelea kuhudumu katika taasisi mbalimbali za ndani na nje ya nchi.

Pia amesema ushiriki wa wanawake katika taaluma ya urubani unaongezeka kwa kasi, huku idadi yao ikielekea kufikia uwiano unaokaribiana na ule wa wanaume, jambo linaloashiria kuongezeka kwa ushiriki wa wanawake katika taaluma ambazo kwa muda mrefu zilionekana kutawaliwa na wanaume.

Dkt. Mgaya amesisitiza kuwa kuongeza idadi ya wataalamu wa ndani katika sekta ya anga kutaimarisha usalama wa usafiri wa anga, kupunguza gharama za kuajiri wataalamu kutoka nje na kuiwezesha Tanzania kujenga uwezo wake wa kitaalamu kadri sekta hiyo inavyoendelea kukua.






Mkurugenzi Mtendaji wa Stanbic Bank Tanzania, Manzi Rwegasira, atajumuika na viongozi wa kimataifa, mawaziri, watunga sera, wawekezaji, taasisi za fedha za maendeleo pamoja na viongozi wa biashara katika Mkutano wa Infra for Africa Forum 2026, unaofanyika jijini Dar es Salaam kuanzia tarehe 5 hadi 6 Agosti 2026.

Mkutano huo, ulioandaliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Africa50, utawakutanisha wadau muhimu kujadili mbinu bunifu za kuharakisha maendeleo na uwekezaji katika miundombinu barani Afrika, huku Mgeni Rasmi akiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Tarehe 5 Agosti, Rwegasira atashiriki katika mjadala wa ngazi ya juu wenye mada “Reinvesting for Expansion: Asset Recycling as a Multiplier”, akiwa pamoja na Mkuu wa Kitengo cha Nishati na Miundombinu Duniani wa Standard Bank Group, Dele Kuti, na viongozi wengine waandamizi. 

Katika mjadala huo atazungumzia ugharamiaji wa miundombinu, uhamasishaji wa mitaji na ushirikiano wa kimkakati unaolenga kuharakisha uwekezaji katika miundombinu barani Afrika.

Tarehe 6 Agosti, pia atazungumza katika kikao cha jumla chenye mada “Pace Setters: African-Designed, African-Led”, sambamba na viongozi waandamizi kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Ecobank, ATIDI na Mfuko wa Uwekezaji wa Taifa wa Angola. 

Kikao hicho kitachambua namna taasisi za fedha za Afrika, wawekezaji wa kitaifa, benki na wadau wa miundombinu wanavyoweza kuhamasisha mitaji ya ndani, kuimarisha mifumo ya kupunguza hatari na kuharakisha ugharamiaji wa miundombinu kupitia suluhu zinazoongozwa na Waafrika.

Stanbic Bank Tanzania inaeleza kuwa maendeleo ya miundombinu yanaendelea kuwa kichocheo muhimu cha ukuaji wa uchumi, mtangamano wa kikanda na ustawi wa muda mrefu, huku ikisisitiza dhamira yake ya kuunga mkono maendeleo endelevu kupitia suluhu bunifu za kifedha na ushirikiano wa kimkakati unaochochea ajenda ya maendeleo ya Tanzania na ukuaji wa Afrika.



Na Mwandishi Wetu

WIZARA ya Maliasili na Utalii kupitia Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), kwa kushirikiana na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki pamoja na Tanzania Safari Channel, imemkaribisha na kumpokea nchini Tanzania mhamasishaji wa amani duniani na mpiga hatua wa kimataifa, Saddam Suleiman Ali Alaya, anayetekeleza safari ya kihistoria ya The World’s Longest Peace Walk. 

Saddam ameingia nchini kupitia Mpaka wa Kasesya uliopo Wilaya ya Kalambo, mkoani Rukwa, akianzia rasmi hatua ya safari yake ya takribani siku 35 nchini Tanzania.

 Katika kipindi hicho atapita katika mikoa ya Rukwa, Katavi na Kigoma kabla ya kuondoka kupitia Mpaka wa Manyovu, akiwa na dhamira ya kuhamasisha amani, mshikamano wa kimataifa na kuitangaza Tanzania kama moja ya vivutio bora vya utalii duniani.  

Safari hiyo  sehemu ya mradi wa kimataifa unaolenga kutembea zaidi ya kilomita 23,000 kutoka Cape Town, Afrika Kusini hadi Magadan, Urusi, kupitia nchi 18 kati ya mwaka 2026 na 2028.

 Tanzania ni nchi ya tano katika historia ya safari hiyo, jambo linaloipa fursa ya kipekee ya kuonesha urithi wake wa asili, utamaduni na ukarimu kwa hadhira ya kimataifa. 

Kwa mujibu wa waratibu wa mradi huo, safari inaungwa mkono na kampeni kubwa ya kimataifa ya vyombo vya habari, utengenezaji wa makala maalumu na ushirikiano na mitandao mbalimbali ya kimataifa inayotarajiwa kufikia zaidi ya watu milioni 480 duniani, huku pia ikilenga kuweka rekodi saba za Guinness World Records. 

Kupitia ushirikiano huu, Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia TTB inaendelea kutumia majukwaa ya kimataifa kuitangaza Tanzania kama kitovu cha utalii, amani na urithi wa dunia, huku ikiwakaribisha wageni kutoka kila pembe ya dunia kutembelea vivutio vya kipekee vya nchi.








Afisa Masoko wa Chama Kikuu cha Ushirika cha Wilaya ya Mbinga (MBIFACU), Osmund Mbunda, amesema chama hicho kinaendelea kuongeza thamani ya zao la kahawa kwa kusindika na kuuza kahawa iliyotayari kwa matumizi badala ya kutegemea uuzaji wa kahawa ghafi pekee. 

Mbunda ameyasema hayo Agosti 3, 2026, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika banda la MBIFACU kwenye Maonesho ya Kilimo Nanenane Kitaifa yanayoendelea jijini Dodoma.

Amesema MBIFACU kwa sasa huuza kahawa katika aina mbalimbali ikiwemo kahawa kavu, kahawa safi na kahawa iliyoongezwa thamani kwa kusindikwa, hatua inayolenga kuongeza mapato ya chama na wakulima pamoja na kuwafanya Watanzania kutumia kahawa zaidi badala ya chai.

Ameongeza kuwa kuongeza thamani ya kahawa ni njia muhimu ya kukuza soko la ndani na kuongeza ushindani wa bidhaa za kahawa katika masoko mbalimbali.

Mbunda amesema ubora wa kahawa unaanzia shambani na si sokoni, hivyo amewahimiza wakulima kuzingatia kanuni bora za uzalishaji kuanzia hatua za awali ili kupata kahawa yenye viwango vinavyokubalika.

Ameongeza kuwa MBIFACU inalenga kuhakikisha Wilaya ya Mbinga na Mkoa wa Ruvuma vinaendelea kuwa vinara wa uzalishaji wa kahawa aina ya Arabica nchini ifikapo mwaka 2050, akibainisha kuwa Ruvuma kwa sasa ndiyo mkoa unaoongoza kwa uzalishaji wa Arabica na unashika nafasi ya pili kitaifa kwa uzalishaji wa kahawa baada ya Mkoa wa Kagera unaozalisha kahawa aina ya Robusta.

Amewaalika wananchi, wakulima na wadau wengine kutembelea Banda la MBIFACU lililopo katika Kijiji cha ushirika kwenye viwanja vya Nanenane Dodoma.



Na Belinda Joseph-Dodoma.

Chama Kikuu cha Ushirika cha Wilaya ya Mbinga (MBIFACU) mkoani Ruvuma kinatarajia kukusanya tani 27,000 za kahawa katika msimu wa mwaka 2026/2027, ikiwa ni ongezeko kutoka tani 24,000 zilizokusanywa msimu wa 2025/2026, kufuatia kuongezeka kwa mashamba yaliyopandwa miaka miwili iliyopita pamoja na wakulima wengi kuhamasika kuboresha mashamba yao kutokana na matarajio ya kuendelea kuwepo kwa bei nzuri ya kahawa sokoni.

Akizungumza katika Maonesho ya Kilimo Nanenane Kitaifa yanayoendelea jijini Dodoma, Agosti 3, 2026, Meneja Mkuu wa MBIFACU, Faraja Komba, amesema katika msimu wa 2025/2026 chama hicho kilisimamia uzalishaji wa tani 24,000 za kahawa kupitia vyama vya ushirika vinavyounda MBIFACU na kahawa hiyo iliuzwa kwa wastani wa shilingi 12,000 kwa kilo na kuwaingizia wakulima zaidi ya shilingi bilioni 282 zilizolipwa moja kwa moja, jambo lililowawezesha kupata faida kubwa kutokana na bei nzuri ya kahawa.

Amesema matarajio ya kukusanya tani 27,000 msimu huu yanatokana na mashamba yaliyopandwa miaka miwili iliyopita kuanza kuvunwa pamoja na wakulima wengi kuhamasika kuboresha mashamba yao, ameongeza kuwa matarajio ya bei ya kahawa yanaendelea kuwa mazuri kutokana na ubora wa kahawa inayozalishwa na wakulima wa MBIFACU.

Akizungumzia kaulimbiu ya Nanenane 2026 isemayo "Tambua Soko, Zalisha kwa Tija na Tekeleza Dira ya Taifa ya 2050," amesema MBIFACU imeamua kushiriki maonesho hayo ili kutangaza bidhaa zake, kutafuta masoko mapya na kuwafikia wadau mbalimbali wa sekta ya kahawa, amesema chama hicho huzalisha kahawa aina ya Arabica katika Wilaya ya Mbinga kwa wastani wa tani kati ya 25,000 na 30,000 kila mwaka.

Aidha, ameeleza kuwa MBIFACU inaendelea kuwahamasisha wakulima kuzalisha kwa tija kwa kuzingatia ubora wa mazao kuanzia shambani, kuongeza uzalishaji kulingana na ukubwa wa mashamba na kupunguza gharama za uzalishaji ili kuongeza kipato cha mkulima.

Pia amesema kupitia banda la MBIFACU katika maonesho hayo, wakulima na wananchi wanapata elimu kuhusu uzalishaji bora wa kahawa na mbinu za kuongeza thamani ya zao hilo, huku chama hicho kikijipanga kuwashirikisha zaidi wanawake na vijana katika uzalishaji wa kahawa ili kutekeleza Dira ya Taifa ya 2050.

Kwa upande wake, Afisa Masoko wa MBIFACU, Osmund Mbunda, amesema chama hicho kimefanikiwa kuongeza thamani ya kahawa kwa kusindika na kuuza kahawa iliyotayari kwa matumizi badala ya kuuza kahawa ghafi pekee, amesema MBIFACU huuza kahawa kavu, kahawa safi na kahawa iliyoongezwa thamani kwa kusindikwa, huku ikiendelea kuwahamasisha wakulima kutumia kahawa zaidi badala ya chai.

Mbunda amebainisha kuwa, ubora wa kahawa unaanzia shambani na siyo sokoni, hivyo wakulima wanapaswa kuzingatia kanuni bora za uzalishaji tangu hatua za awali.

Ameongeza kuwa lengo la MBIFACU ni kuhakikisha Wilaya ya Mbinga na Mkoa wa Ruvuma vinaendelea kuongoza uzalishaji wa kahawa aina ya Arabica nchini ifikapo mwaka 2050, akibainisha kuwa kwa sasa Ruvuma ndiyo mkoa unaoongoza kwa uzalishaji wa Arabica nchini na unashika nafasi ya pili kitaifa kwa uzalishaji wa kahawa baada ya Mkoa wa Kagera unaozalisha kahawa aina ya Robusta.

Kwa upande wake, Mrajis wa Vyama vya Ushirika Mkoa wa Ruvuma, Venance Msafiri, amesema wakulima wa kahawa mkoani Ruvuma wameendelea kunufaika na mauzo ya kahawa kupitia vyama vya ushirika, hali iliyochangia kuongeza kipato cha wakulima mmoja mmoja na kuboresha uchumi wa mkoa kwa ujumla.

Amesema mfumo wa ushirika umeendelea kuwawezesha wakulima kupata soko la uhakika, malipo kwa wakati na bei nzuri ya kahawa, jambo lililoongeza ari ya wakulima kuendelea kuwekeza katika uzalishaji wa zao hilo, aidha amewahimiza wakulima kuendelea kutumia vyama vya ushirika kama chombo cha kuimarisha masoko ya mazao yao na kuongeza tija katika uzalishaji wa kahawa.


Na Belinda Joseph.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Ukaguzi na Usimamizi wa Vyama vya Ushirika Tanzania (COASCO), CPA Jeremia Jackson Mugeta, amesema shirika hilo limepokea na liko tayari kutekeleza maagizo yaliyotolewa na Makamu wa Rais, Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, ya kuhakikisha linavikagua na kuvisimamia vyama vya ushirika pamoja na kuwasilisha taarifa kuhusu hali ya ushirika nchini.

CPA Mugeta amesema hayo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya maadhimisho ya Siku ya Ushirika yaliyofanyika katika Kijiji cha Ushirika ndani ya viwanja vya Maonesho ya Nanenane kitaifa jijini Dodoma Agosti 3, 2026.

Ameeleza kuwa katika mwaka wa fedha 2026/2027 shirika hilo lilianza maandalizi ya ukaguzi kuanzia Julai 20 kwa kuandaa mpango kazi, huku wataalamu wakiendelea kuratibu zoezi hilo ambalo litahusisha vyama vyote vya ushirika vilivyofunga hesabu zake Machi 31, 2026.

Amefafanua kuwa kwa mujibu wa sheria, vyama vya ushirika vinapofunga hesabu zake hupewa miezi mitatu kuandaa na kuwasilisha taarifa za fedha kwa mkaguzi wa nje ambaye ni COASCO, na kwamba mara baada ya maonesho ya Nanenane wakaguzi wataanza kwenda katika maeneo ya vyama hivyo kwa ajili ya kufanya ukaguzi.

CPA Mugeta amesema COASCO itatekeleza maagizo yote yaliyotolewa na Makamu wa Rais na kuwasilisha taarifa kwa mamlaka husika kulingana na ratiba ya kisheria, ambapo ripoti ya kwanza itawasilishwa mwezi Januari 2027 kwa Waziri wa Kilimo baada ya kukamilika kwa kipindi cha miezi sita.

Amesema katika mwaka wa fedha uliopita COASCO ilikuwa na lengo la kukagua takribani vyama 5,000 vya ushirika, ambapo ilifanikiwa kukagua vyama 4,858, huku lengo la mwaka wa fedha 2026/2027 likiwa ni kukagua vyama vyote vya ushirika nchini.

Aidha, ametoa wito kwa vyama vya ushirika kuzingatia sheria kwa kufunga hesabu zao kwa wakati na kuziwasilisha kwa COASCO kwa ajili ya ukaguzi.

Amesisitiza kuwa mafanikio ya zoezi hilo yanategemea ushirikiano wa kila chama cha ushirika kutekeleza wajibu wake kwa mujibu wa sheria, akionya kuwa vyama vitakavyokiuka taratibu na sheria vitachukuliwa hatua na Mrajis wa Vyama vya Ushirika.



 Na: Mwandishi wetu - Dodoma

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Mwigulu Lameck Nchemba ameipongeza Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viatilifu Tanzania (TPHPA) kwa kazi nzuri ya kuhifadhi mbegu za asili na kupambana na wadudu na magonjwa ya mimea na hivyo kuchangia utoshelevu wa chakula na kuongeza mapato.

Mkurugenzi Mkuu wa TPHPA Prof. Joseph Ndunguru akitoa maelezo kwa waziri Mkuu wakati alipotembelea banda hilo kwenye maonesho wa wakulima Nanenane Jijini Dodoma.

Pongezi hizo amezitoa wakati alipotembelea banda TPHPA kabla ya kufungua rasmi maonesho ya wakulima Nanenane kitaifa Jijini Dodoma na kuelezwa kazi mbalimbali ambazo zinatekelezwa na mamlaka hiyo zinazoleta tija kwenye maendeleo ya sekta ya kilimo na biashara ya uuzaji mazao nje ya nchi.

“Nawapongeza kwa kazi nzuri mnayoifanya katika kusaidia kutimiza malengo ya Serikali hasa katika eneo la sekta ya kilimo ambayo inaajiri Watanzania wengi kuliko sekta nyingine yoyote, endeeeni kuchapa kazi nasi kwa upande wetu kama Serikali tutaendelea kuwaunga mkono katika kuboresha mazingira ya kazi zenu kwa kuwapatia vifaa na mahitaji mengine muhimu ili kuongeza tija” alisema Mhe. Nchemba.

Awali akitoa maelezo ya kazi za Mamlaka hiyo kwa Waziri Mkuu, Mkurugenzi Mkuu wa TPHPA Prof. Joseph Ndunguru amesema pamoja na majukumu mengi waliyonayo lakini wanasaida kuhakikisha mazao yanayozalishwa na wakulima nchini yanapimwa ubora wake na kufikia viwango vinavyohitaji kwenye masoko mbalimbali duniani na hivyo kuingizia taifa fedha za kigeni.

“Ili makampuni mbalimbali kutoka Tanzania yaweze kuuza mazao kwenye masoko mbalimbali nje ya nchi kuna vigezo ambavyo masoko hayo yanahitaji kwenye mazao hayo, hivyo sisi kama mamlaka tunasaidia kuhakikisha makampuni hayo yanapata bidhaa zenye kukidhi viwango hivyo na hivyo kuwezesha kufikia soko kulingana na mahitaji ya kila soko na bidhaa inapouzwa” alieleza Prof. Ndunguru.

Prof. Ndunguru amesema pia jukumu hilo linakwenda sambamba na kudhibiti visumbufu vya mazao ikiwemo Magonjwa na wadudu waharibifu wa mazao ili wakulima waweze kulima kilimo chenya tija na kazi hiyo inafanywa kwa kutumia teknolojia za kisasa kabisa za utambuzi na udhibiti ikiwemo kipimo cha Vinasaba (DNA) ambacho kinauwezo wa kupima kinasaba cha kiumbe chochote  na kutoa majibu ndani ya dakika 20.

“Teknolojia hii ya kisasa tunaenda nayo mahali popote huko kwenye mshamba ya wakulima, tunachukua sampuli na kupima hapohapo shambani mkulima akiona na ndani ya dakika 20 tunapata majibu kuwa ni Kirusi gani, Bakteria gani au Fangasi yupi na kupendekeza kiuatilifu gani au mbinu gani sahihi inafaa kutumika kutatua changamoto iliyoonekana” alifafanua Mkurugenzi huyo Mkuu wa TPHPA Prof. Ndunguru.

Aidha amesema kuwa kazi nyingine ambayo TPHPA inafanya ni kutunza nasaba za mimea kwa maana ya Mbegu za asili zote na mpaka sasa benki hiyo ya mbegu ina aina elfu kumi (10,000) zimetuzwa  kutoka mikoa mbalimbali na za mazao aina mbalimbali zile za asili kabisa zinazotambuliwa na jamii na zingine zilikuwa zinaelekea kupotea lakini wamefanikiwa kuzitunza.

Pia Prof. Ndunguru amesema jukumu lingine muhimu la mamlaka hiyo ni kutoa mafunzo ya matumizi salama ya Viuatilifu pamoja na kuangalia ubora wa Viuatilifu vilivyopo na vile vinavyoingia nchini kwa kutumia mitambo na vifaa vya kisasa vilivyopo makao makuu ya TPHPA pale Arusha na kwenye ofisi za kanda ya mamlaka hiyo ili kusaidia wakulima kupata viuatilifu salama na kuvitumia kwa usahihi bila kuleta adhari kwao, mazao na mazingira.

“Kupitia jukumu hilo Mamlaka imeiongezea Serikali mapato katika mizigo ambayo inasafirishwa kutoka nchini kwenda nje ya nchi lakini pia kufanikiwa kufungua masoko mbalimbali ya bidhaa ambayo nchi yetu ilifungiwa kutokana na kutokidhi mahitaji ya masoko yao na sasa watanzania na makampuni yanauza mazao yetu kwa wingi kwenye masoko hayo “alifafanua Prof. Ndunguru.

Mamlaka ya Afya ya mimea na Viuatilifu Tanzania TPHPA inashiriki kwenye maonesho ya wakulima Nanenane kwenye kanda zote ikiwemo Pwani, Kanda ya kati Dodoma, Kanda ya Kaskazini jijini Arusha, Kanda ya Kusiki Mbeya na Kanda ya Magharibi Simiyu.


MATUKIO KATIKA PICHA WAZIRI MKUU ALIPOTEMBEA BANDA LA TPHPA KWENYE MAONESHO HAYO.









 

 

 

 

 


Top News