Na Karama Kenyunko Michuzi Tv

MAMLAKA ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Kituo cha Hali ya Hewa cha Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), imeadhimisha Siku ya Hali ya Hewa Duniani kwa kutoa elimu kwa wadau pamoja na kuweka mipango ya kuendelea kutoa huduma bora, kuongeza tija na ufanisi, na kuhakikisha usalama wa usafiri wa anga kwa kutoa taarifa sahihi.

Akizungumza leo, Machi 23, 2026, jijini Dar es Salaam wakati wa kutoa elimu kwa wanafunzi wa shule mbalimbali za msingi waliotembelea Kituo cha Hali ya Hewa cha JNIA, Meneja wa TMA wa Huduma za Hali ya Hewa katika Usafiri wa Anga na Msimamizi wa Kituo cha Hali ya Hewa JNIA, John Mayunga, amesema kuwa ni muhimu kuelimisha jamii ili iweze kuchukua tahadhari na kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa.

Mayunga ameongeza kuwa kuna mchango mkubwa wa utoaji wa tahadhari mapema kabla jamii haijakumbwa na athari za mabadiliko ya hali ya hewa, kwani majanga mengi duniani yamehusishwa na hali mbaya ya hewa.

“Serikali imeendelea kufanya uwekezaji mkubwa wa kimkakati katika huduma za hali ya hewa kwa kununua vifaa vya kisasa pamoja na kuajiri wataalamu, jambo ambalo limesaidia kupata taarifa sahihi za hali ya hewa kwa ajili ya matumizi mbalimbali ya wadau na kijamii,” amesema Mayunga.

Aidha, Mayunga amesisitiza umuhimu wa kuwajengea uwezo vijana kwa kuzingatia umuhimu wa taarifa za hali ya hewa, kwani wao ni taifa la kesho, huku akifafanua kuwa TMA ni miongoni mwa taasisi za kwanza barani Afrika kupata cheti cha ubora katika huduma za hali ya hewa kwa usafiri wa anga.

Kwa upande wake, Msimamizi wa Kituo cha Uangazi TMA–JNIA, Ally Selemani, amesema wanajivunia kutumia teknolojia ya kisasa iliyowawezesha kutoa taarifa za uhakika za hali ya hewa na kupunguza changamoto kwa kiwango kikubwa katika utendaji wa kazi.

Kwa upande wao, baadhi ya wanafunzi, Shaneli Kaguli na Isabela Dany kutoka Shule ya Msingi Daddy, wameishukuru TMA kwa kuwaelimisha kuhusu utendaji wa kazi zao, jambo linalowasaidia kuwa na uelewa zaidi kuhusu matumizi ya taarifa za hali ya hewa na namna ya kukabiliana na athari zinazoweza kutokea.

Maadhimisho ya Siku ya Hali ya Hewa Duniani 2026 yamebeba kaulimbiu isemayo: “Pima hali ya hewa leo, ili kesho iwe salama”





Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Mahmoud Thabit Kombo (Mb) amewasilisha taarifa ya utekelezaji wa Mpango wa Bajeti wa mwaka 2025/2026 na mpango wa bajeti wa mwaka wa Fedha 2026/2027 kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ulinzi na Usalama (NUU) jijini Dodoma.

Akiwasilisha taarifa hiyo, Balozi Kombo alieleza hatua mbalimbali zilizofikiwa na wizara katika kutekeleza majukumu yake, ikiwemo kuimarisha diplomasia ya uchumi, kulinda maslahi ya Taifa na kukuza ushirikiano wa uwili, kikanda na kimataifa.

Katika taarifa hiyo, Mhe. Balozi Kombo alibainisha mafanikio yaliyopatikana kupitia ushiriki wa Tanzania katika majukwaa ya kimataifa na kikanda na juhudi za kuvutia uwekezaji na kupanua fursa za biashara kwa Watanzania.

Alisisitiza umuhimu wa kuendelea kuelimisha wadau kuhusu fursa zitokanazo na uhusiano wa kimataifa na hivyo kuleta tija ya diplomasia ya uchumi nchini.

Kuhusu mpango wa bajeti wa mwaka 26/27, Waziri Kombo alieleza kuwa vipaumbele vya Wizara vitaendelea kutekelezwa kwa kuzingatia miongozo ya kitaifa, kikanda na kimataifa, Sera ya Mambo ya Nje; Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050; Dira ya Maendeleo ya Zanzibar 2050; Mpango wa Nne wa Taifa waMaendeleo wa Miaka Mitano (26/27 - 30/31); Mpango wa Maendeleo wa Zanzibar(2021 – 2026); Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya Uchaguzi ya 2025; Mkataba wa Uanzishwaji wa Jumuiya ya Afrika Mashariki wa mwaka 1999; Mkataba wa Uanzishwaji wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika wa mwaka 1992; Ajenda ya Mwaka 2030 ya Umoja wa Mataifa kuhusu Maendeleo Endelevu; Ajenda ya Mwaka 2063 ya Umoja wa Afrika; Dira ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika ya Mwaka 2050; Dira ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Mwaka 2050; na mikataba mingine ya Kikanda na Kimataifa.

Alitaja vipaumbele vya Wizara kwa mwaka wa fedha 2026/2027 kuwa ni Kuendelea kuimarisha uratibu na ushirikiano wa uwili, kikanda na kimataifa; Kuratibu utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje hususan utekelezaji wa diplomasia ya uchumi; Kulinda Taswira, heshima na kutetea maslahi ya Taifa letu katika nyanja ya kimataifa; na Kuboresha mazingira ya utendaji kazi kwa watumishi wa Wizara, kuimarisha utawala bora na rasilimali watu pamoja na kutekeleza miradi ya maendeleo ya Wizara na taasisi zake.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ulinzi na Usalama Mhe. Najma Giga (Mb) aliipongeza Wizara kwa uwasilishaji wa taarifa hiyo kwa ufasaha.

Alieleza kuwa Kamati hiyo itaendelea kushirikiana na Wizara ili iendelee kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kwamba kukiwa na jambo linalowahitaji wawasiliane ili kujadili kwa pamoja na kuona jinsi ya kulitanzua kwa pamoja








Na Mwandishi wetu

Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bw. Yusuph Mwenda, amezitaka kampuni za Kichina na wafanyabiashara wote nchini kuzingatia kikamilifu sheria za kodi kwa kulipa kwa wakati, kutoa taarifa sahihi, na kushirikiana kwa karibu na mamlaka hiyo.

Akizungumza katika Mkutano wa Mafunzo na Kubadilishana Uzoefu wa Kodi kati ya Biashara za Tanzania na China 2026 uliofanyika jijini Dar es Salaam, Mwenda alisema kuwa ni wajibu wa kila kampuni—iwe ya binafsi au ya Serikali—kufuata taratibu za kodi kwa uaminifu, ikiwa ni pamoja na kutumia mifumo ya kidijitali katika usajili na ulipaji wa kodi.

Alisisitiza umuhimu wa uwazi na usawa katika utekelezaji wa majukumu ya kikodi, akibainisha kuwa uratibu mzuri kati ya TRA na walipa kodi utasaidia kuepusha migongano isiyo ya lazima.

“Tunathamini mchango wa wawekezaji katika maendeleo ya taifa na tunaahidi kuendelea kushirikiana nanyi kwa uwazi na ushirikiano endelevu,” alisema Mwenda.

Kwa upande wake, Balozi wa China nchini Tanzania, Bi. Chen Mingjian, alizitaka kampuni za Kichina zinazofanya biashara nchini kuzingatia kikamilifu sheria na kanuni za kodi za Tanzania, kulipa kodi stahiki, na kuepuka vitendo vya ukwepaji kodi.

Alisisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya kampuni hizo na TRA ili kuhakikisha uwazi na ufanisi katika ukusanyaji wa mapato ya Serikali.

Aidha, Balozi Chen alieleza kuwa matumizi ya mifumo ya kisasa ya TEHAMA yanawezesha kampuni kupata taarifa sahihi na za wakati kuhusu masuala ya kodi, hatua inayosaidia kupunguza changamoto zilizokuwepo hapo awali.

Aliongeza kuwa juhudi hizo zinaendana na azma ya Serikali ya Tanzania ya kuboresha mazingira ya uwekezaji na biashara, akirejea pia mpango wa maboresho ya mfumo wa kodi uliotangazwa hivi karibuni unaojumuisha mapendekezo 284, wenye lengo la kuufanya mfumo huo kuwa wa kisasa zaidi, rafiki kwa walipa kodi, na wenye ufanisi mkubwa katika utoaji wa huduma.








Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma

Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt. Tausi Kida, amefungua mkutano wa kitaifa unaowakutanisha wadau wa taasisi za utafiti kwa lengo la kujadili namna bora ya kuoanisha tafiti na mchakato wa upangaji wa maendeleo ya taifa.

Mkutano huo wa siku mbili umeanza Machi 23, 2026 jijini Dodoma, ukihusisha watafiti, watunga sera na wadau mbalimbali wa maendeleo.

Akizungumza wakati wa ufunguzi, Dkt. Kida amesema Tanzania ipo katika hatua muhimu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, inayolenga kujenga uchumi wa thamani ya trilioni moja pamoja na kuboresha ustawi wa wananchi.

Amefafanua kuwa dira hiyo inalenga pia kutokomeza umasikini uliokithiri, kupunguza vifo vya akina mama vitokanavyo na uzazi, na kupunguza vifo vya watoto wachanga ifikapo mwaka 2050.

“Tutahakikisha hakuna Mtanzania atakayebaki katika umasikini uliokithiri, huku tukiboresha huduma muhimu za kijamii kama afya na elimu,” amesema Dkt. Kida.

Aidha, ameeleza kuwa utekelezaji wa dira hiyo utaongozwa na mipango ya muda mrefu itakayogawanywa katika vipindi vya miaka mitano mitano, huku kila mwaka ukiwa na mpango mahsusi wa utekelezaji wenye vipaumbele vya kitaifa.

Amesema Tume ya Taifa ya Mipango itaendelea kuwa mshauri mkuu wa Serikali katika masuala ya uchumi na maendeleo, sambamba na kusimamia na kuratibu utekelezaji wa mipango hiyo.

Akigusia umuhimu wa tafiti, Dkt. Kida amesisitiza kuwa tafiti za kiuchumi na kijamii ni nyenzo muhimu katika kubuni sera bora, kuimarisha utekelezaji wa mipango, na kufikia malengo ya maendeleo ya taifa.

“Ni muhimu kuwa na mwongozo madhubuti wa tafiti unaozingatia vipaumbele vya taifa ili kuhakikisha matokeo yake yanatatua changamoto halisi za wananchi,” amesisitiza.

Katika kuimarisha ushirikiano na wadau wa utafiti, Dkt. Kida amesema Tume ya Taifa ya Mipango inapanga kuanzisha mfumo wa kidijitali (portal) wa kuhifadhi na kusambaza tafiti zote zinazofanyika nchini, ili kuhakikisha zinatumika kikamilifu katika maamuzi ya kisera na mipango ya maendeleo.

Ameongeza kuwa tafiti hizo zitakuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya uchumi, jamii na mazingira, hasa katika kukabiliana na changamoto zinazoibuka kama ongezeko la idadi ya watu na mabadiliko ya tabianchi.

Mkutano huo unalenga kujenga uelewa wa pamoja na kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali na taasisi za utafiti, ili kuhakikisha tafiti zinazofanyika nchini zinaendana na vipaumbele vya maendeleo ya taifa.

Kwa ujumla, Tanzania inaendelea kujipanga kwa mageuzi makubwa ya kiuchumi na kijamii, yakilenga kujenga uchumi shindani na jumuishi, kuongeza ajira na tija, pamoja na kuimarisha mchango wa sekta binafsi katika maendeleo ya taifa.




 


Asema nchi ina usalama mkubwa wa mafuta hivyo wananchi waendelee kupata huduma muda wote

Timu maalum kuundwa kufuatilia uingizaji wa mafuta nchini


WAZIRI wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi ameitaka Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kuhakikisha kuwa, hakuna mfanyabiashara anayeficha mafuta kwa kisingizio cha kusubiri bei za mafuta zipande kutokana na mgogoro unaoendelea katika eneo la Mashariki ya Kati ambao umepelekea baadhi ya nchi kukumbana na changamoto za upatikanaji wa mafuta.

Akizungumza jijini Dodoma katika kikao na Taasisi za Wizara zinazosimamia Sekta ya Mafuta, Mhe. Ndejembi ameeleza kuwa nchi ina usalama mkubwa wa mafuta na kwamba Serikali imejipanga vizuri kuhakikisha wananchi katika maeneo yote wanapata huduma bila vikwazo hivyo EWURA anapaswa kuhakikisha hakuna mafuta yanayofichwa katika maghala ya kuhifadhi Mafuta.

Aidha, ili kuhakikisha mafuta yote yaliyoagizwa nje ya nchi yanafika nchini kwa mujibu wa mkataba, Mhe. Ndejembi ameelekeza kuundwa kwa timu maalum kufuatilia mwenendo wa uingizaji wa Mafuta nchini ambayo itahusisha Wataalam kutoka Wakala wa Uagizaji wa Mafuta kwa Pamoja (PBPA), EWURA, Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) pamoja na Ulinzi na Usalama.

" Timu hii itakuwa na jukumu la kufuatilia hatua kwa hatua na kuhakikisha kuwa mafuta yote yaliyoagizwa ambayo yako njiani kuja nchini yanafika kwa wakati bila kikwazo wala changamoto yoyote. Hali ya biashara ya mafuta huko duniani si ya kuridhisha, baadhi ya nchi bei ya mafuta imepanda maradufu na wafanyabiashara wengine wanaweza kuingia tamaa na kupeleka mafuta huko, katika hili sitarajii kuona mikataba tuliyoingia na waagizaji wa mafuta ikikiukwa." Amesisitiza Mhe. Ndejembi

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi Asilia, Dkt. James Mataragio, amewahakikishia Watanzania kuwa nchi ina akiba ya kutosha ya mafuta hadi mwezi Julai 2026.

Amesema Serikali ilichukua hatua za mapema kwa kushirikiana na taasisi zake, ili kuhakikisha kunakuwa na uhakika wa upatikanaji wa mafuta na kwa gharama himilivu.

Ameongeza kuwa Wizara itaendelea kusimamia Taasisi zake ili kuhakikisha mafuta yaliyopo njiani yanafika kwa wakati, pamoja na kuwadhibiti wauzaji ili wasitumie changamoto iliyopo kama fursa ya kupandisha bei.

Awali, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Uagizaji wa Mafuta kwa Pamoja (PBPA) Bw. Erasto Simon alieleza kuwa hali ya upatikanaji wa mafuta nchini iko salama ambapo ameeleza kuwa ukijumuisha mafuta yaliyopo nchini na yaliyopo njiani kuna petroli lita milioni 474 inayotosheleza siku 78, dizeli lita milioni 392 inayotosheleza siku 50 pamoja na lita milioni 55 za mafuta ya ndege zinazotosheleza siku 91.

Naye, Mkurugenzi Mtendaji Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) Bw.Mussa Makame ameeleza kuwa kuna mafuta ya kutosha ndani ya nchi na ambayo yako safarini kwani Serikali ilishasaini mikataba na wazabuni mapema kwa ajili ya uingizaji wa mafuta.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Dkt. James Andilile ameeleza kuwa kwa sasa soko liko sawa hakuna mfumuko wa bei hivyo EWURA itahakikisha watu hawafichi mafuta kusubiri mfumuko wa bei katika soko la dunia.

Amesema EWURA imeendela kushirikiana na wadau wa mafuta wakiwemo waagizaji na wauzaji ili kuhakikisha kama kuna changamoto zozote zinatatuliwa kwa haraka ili wananchi wapate huduma kwa uhakika.



Ikulu Zanzibar | 23 Machi 2026
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amekutana na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL), Ndugu David Nchimbi, aliyeambatana na Mkurugenzi Mkuu wa TTCL, CPA Moremi Marwa, pamoja na ujumbe wao, waliofika kujitambulisha.

Rais Dkt. Mwinyi ameahidi kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na TTCL katika kuimarisha mawasiliano Zanzibar kupitia huduma mbalimbali zinazotolewa na Shirika hilo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya TTCL, Ndugu David Nchimbi, amemshukuru Rais Dkt. Mwinyi kwa ushirikiano unaoendelea kati ya Shirika hilo na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha huduma za mawasiliano nchini.

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Dkt. Jim Yonazi amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mtendaji mpya wa Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS) Dkt. Adam Joseph Mrisho ambaye amefika kujitambulisha baada ya kuteuliwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kikao hicho kimefanyika tarehe 23 Machi, 2026 katika Ofisi ya Waziri Mkuu iliyopo mtaa wa Reli jijini Dodoma na kudhuriwa na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) Dkt. James Kilabuko pamoja na Mratibu wa Masuala ya UKIMWI Bi. Adela Mpina.

Dkt.Yonazi ameahidi kumpa ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu yake ya kila siku. (PICHA ZOTE NA OFISI YA WAZIRI MKUU).











Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeweka wazi kuwa itaendelea kushirikiana na Austria katika kuimarisha mahusiano ya kidiplomasia yanayolenga kuleta tija ya kiuchumi na usalama wa jamii.

Hayo yameelezwa Machi 23, 2026, jijini Dar es Salaam wakati wa mazungumzo kati ya Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Mhe. Ayoub Mahmoud (Mb), na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Austria anayeshughulikia masuala ya kisiasa, Mhe. Balozi Dkt. Hannah Liko.

Mazungumzo hayo yalijikita katika kuainisha vipaumbele vya Tanzania ndani ya Mkakati mpya wa Austria kwa Afrika (2026–2029), mkakati ambao unasisitiza ushirikiano wa usawa, ulinzi wa haki za binadamu, na utawala wa sheria kama nguzo kuu za kuelekea maendeleo endelevu.

Kuelekea utekelezaji wa mkakati huo, Mhe. Mahmoud amewasilisha vipaumbele vya Wizara vinavyolenga kuimarisha usalama na uwezo wa kukabiliana na majanga, huku mkazo mkubwa ukiwekwa katika kupambana na uhamiaji haramu, biashara haramu ya binadamu, matumizi ya dawa za kulevya, pamoja na kuzuia uhalifu wa kimtandao ambao umekuwa tishio la kimataifa.

Mhe. Mahmoud amezungumzia mfumo wa Triple-Win, unaolenga kudhibiti uhamiaji haramu huku ukifungua milango ya kisheria kwa vijana wa Kitanzania wenye ujuzi kupata ajira na mafunzo ya ufundi stadi nchini Austria, hatua inayotarajiwa kuwa suluhisho la kudumu katika kuwapatia vijana fursa za kimataifa na kupunguza utegemezi.

Aidha, Tanzania imekaribisha nia ya Austria kuwekeza katika miradi ya nishati safi na uchumi wa kijani kupitia makampuni yake, ili kusaidia mapambano dhidi ya mabadiliko ya tabianchi kupitia miradi ya pamoja ya kitafiti na kiteknolojia.

Kwa upande wake, Dkt. Liko amethibitisha utayari wa Austria kuunga mkono operesheni za kikanda za kulinda amani za Umoja wa Mataifa na kuongeza kuwa Austria itaendelea kuwa mshirika wa kimkakati katika kukuza viwanda, sayansi, na utamaduni ili kuhakikisha Tanzania inabaki kuwa mazingira salama kwa raia, uwekezaji, na utalii kwa manufaa ya mataifa yote mawili.

Vilevile amesema kupitia Shirika la Maendeleo la Austria (ADA), nchi hiyo imeahidi kuendelea kuwa mshirika wa kimkakati wa Tanzania katika kukuza utamaduni, sayansi, na maendeleo ya kijamii.













Top News