Morogoro

Bodi ya Tano ya Ushauri ya Wizara kwa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) imeanza rasmi majukumu yake kwa kufanya kikao cha 47 cha Bodi, ambacho pia ni kikao cha kwanza cha bodi hiyo mpya.

Kikao hicho kimefunguliwa leo Aprili 2, 2026 mkoani Morogoro na Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Luteni Mstaafu Chiku Abdallah Sumbu Gallawa, katika Ukumbi wa Kituo cha Mbegu Bora za Miche ya Miti cha TFS.

Kabla ya kikao hicho, wajumbe walifanya vikao vya kamati kuanzia Machi 31 hadi Aprili 1, 2026, kujadili masuala mbalimbali ya kiutendaji ya wakala.

Pamoja na mambo mengine, Bodi ilipokea na kujadili Mpango wa Biashara wa TFS kwa mwaka wa fedha 2026/2027, sambamba na taarifa mbalimbali za utekelezaji wa majukumu ya taasisi.

Kuanza kwa kikao hicho kunafuatia uzinduzi wa Bodi hiyo uliofanywa Februari 13, 2026 jijini Dodoma na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji.












Benki Kuu ya Tanzania (BoT) imeamua kuendelea kubakiza kiwango chake cha riba ya msingi ya ukopeshaji (benchmark lending rate) katika asilimia 5.75 kwa robo ya pili ya mwaka huu, ikionesha tahadhari kufuatia kuongezeka kwa sintofahamu katika uchumi wa dunia.

Uamuzi huo ulifikiwa katika kikao cha hivi karibuni cha Kamati ya Sera ya Fedha (MPC), ambapo watunga sera walitathmini hatari zinazotokana na mazingira ya kimataifa dhidi ya uimara wa uchumi wa ndani.

Akizungumza kuhusu uamuzi huo, Naibu Gavana wa BoT, Dkt. Yamungu Kayandabila, alisema hatua hiyo inalenga kusawazisha kati ya kukuza uchumi na kudhibiti mfumuko wa bei.

“Haikuwa uamuzi rahisi,” alisema, akieleza kuwa mvutano wa kisiasa unaoendelea katika Mashariki ya Kati umeanza kuathiri mwenendo wa masoko ya dunia.

Alifafanua kuwa mvutano huo umevuruga minyororo ya usambazaji wa bidhaa na kuchangia kupanda kwa bei, hususan mafuta ambayo sasa yamevuka dola za Marekani 100 kwa pipa, juu ya makadirio ya awali.

Katika hatua nyingine, MPC ilitangaza kupunguza wigo wa riba (interest rate corridor) unaozunguka kiwango cha CBR kutoka pointi 200 hadi 150 za msingi (basis points), hatua inayoweka kiwango cha riba ya siku saba kati ya benki katika viwango vya asilimia 4.25 hadi 7.25.

Kwa mujibu wa Dkt. Kayandabila, hatua hiyo inalenga kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa sera ya fedha, huku ikidumisha uthabiti wa bei na kusaidia ukuaji wa uchumi.

Licha ya changamoto za kimataifa, BoT imeeleza kuwa uchumi wa ndani unaendelea kuonesha uimara.

Katika robo ya kwanza ya mwaka, uchumi ulikua kwa asilimia 6.2 Tanzania Bara na asilimia 6.7 Zanzibar, ukichochewa na sekta za ujenzi, kilimo, utalii na huduma za kifedha.

Kwa robo ya pili, ukuaji unatarajiwa kufikia asilimia 6.1 kwa Tanzania Bara na asilimia 6.6 Zanzibar, ingawa hatari za nje zinaweza kuathiri mwenendo huo endapo zitaongezeka.

Kwa upande wa mfumuko wa bei, umeendelea kubaki ndani ya lengo la BoT la asilimia tatu hadi tano. Kwa wastani, ulikuwa asilimia 3.3 Tanzania Bara na asilimia 4.5 Zanzibar, hali iliyochangiwa na utulivu wa bei za chakula pamoja na kiwango cha ubadilishaji fedha.

Hata hivyo, Benki Kuu imeonya kuwa ongezeko la gharama za nishati na usafirishaji linaweza kuongeza shinikizo la mfumuko wa bei katika miezi ijayo.

Katika sekta ya benki, hali imeendelea kuwa imara ambapo kiwango cha mikopo chechefu kimeshuka hadi asilimia 2.9, chini ya kiwango kinachokubalika kisheria, huku benki zikiendelea kuwa na mtaji wa kutosha na ukwasi wa kuridhisha.

Kwa upande wa sekta ya nje, nakisi ya akaunti ya sasa imepungua hadi asilimia 2.2 ya Pato la Taifa (GDP), ikichangiwa na kuongezeka kwa mauzo ya nje ya dhahabu, mazao ya kilimo na huduma za utalii.

Zanzibar nayo imeendelea kufanya vizuri, ikirekodi ziada ya akaunti ya sasa kutokana na mapato ya utalii.

Aidha, akiba ya fedha za kigeni imefikia zaidi ya dola za Marekani bilioni 6.2, kiwango kinachoweza kugharamia uagizaji wa bidhaa kwa karibu miezi mitano, juu ya viwango vya kikanda.

Kwa upande wa mapato ya serikali, makusanyo ya kodi yamevuka malengo kutokana na kuimarika kwa usimamizi na utii wa walipakodi, huku matumizi ya serikali yakiendelea kubaki ndani ya mipaka ya rasilimali zilizopo.

Hata hivyo, MPC imeonya kuwa bado kuna hatari zinazoikabili uchumi.

“Tishio kubwa kwa matarajio ya uchumi ni mzozo unaoendelea Mashariki ya Kati. Endapo utaongezeka, unaweza kuongeza mfumuko wa bei na kupunguza kasi ya ukuaji wa uchumi duniani na nchini,” alisisitiza Dkt. Kayandabila. 










Na Karama Kenyunko Michuzi Tv.

MKURUGENZI Mtendaji wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Kisenge, amesema watu milioni 20 duniani hufariki kila mwaka kutokana na magonjwa ya moyo, huku matumizi ya tumbaku yakitajwa kuwa miongoni mwa visababishi vikuu.

Dkt. Kisenge, ambaye pia ni daktari bingwa wa magonjwa ya moyo, amesema hayo leo Aprili Mosi, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa Uzinduzi wa ripoti inayoonesha namna kampuni za Tambuku nchini zinavyoingilia sera za nchi.

“Kama mnavyofahamu, duniani kote magonjwa ya moyo yanachangia vifo vingi, na kati ya watu milioni 20 wanaopoteza maisha kila mwaka, moja ya visababishi vikuu ni matumizi ya tumbaku au uvutaji wa sigara, ukifuatiwa na shinikizo la damu na kisukari,” amesema.

Amesema matatizo yanayotokana na matumizi ya tumbaku, hasa kwa nchi za Afrika, yameongezeka kwa kasi.

Amesema, nchini Tanzania, uvutaji wa sigara na shisha umeongezeka, hali inayoiweka nchi katika alama nyekundu kutokana na kasi hiyo.

Ameonya kuwa kuvuta shisha mpigo nmoj ni hatari zaidi,kwani ni sawa na kuvuta sigara 100 kwa wakati mmoja, jambo linalosababisha madhara makubwa kwenye mishipa ya damu ya moyo.

“Uvutaji huu husababisha mgando wa damu kwenye mishipa ya moyo, ambao unaweza kusababisha kifo cha ghafla au kiharusi. Pia sigara huathiri mapafu na kusababisha saratani, hivyo hushambulia karibu kila kiungo cha mwili,” amesema.

Ameongeza kuwa JKCI imeweka mikakati mbalimbali ikiwemo kutoa elimu kwa wananchi kuhusu madhara ya sigara na kufungua matawi katika maeneo mbalimbali nchini kwa ajili ya kuwafikia wananchi wengi zaidi.

“Katika mikoa 33 tuliyotembelea, tumekutana na wagonjwa wengi, na kwa kiasi kikubwa chanzo kilikuwa ni matumizi ya sigara,” amesema.

Dkt. Kisenge amesema wagonjwa wengi wameathirika kwa kupata matatizo ya moyo, presha na wengine walihitaji vipimo maalum kutokana na madhara hayo.

Aidha ameishauri serikali kuweka mikakati madhubuti, ikiwemo kuongeza kodi kwenye bidhaa za tumbaku na kutunga sheria kali zitakazodhibiti uvutaji wa sigara, hasa katika maeneo ya mikusanyiko ya watu.


Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Kudhibiti Tumbaku nchini(TTCF), Lutgard Kagaruki amesema kuwa utafiti huo unafanyika kila baada ya miaka miwili na imeanza tangu 2019 na kwamba ripoti hii ni ya awamu ya tano .

Ripoti yetu ni sehemu ya ripoti kubwa ya dunia mwaka huu nchi 100 zilishiriki kwenye huu uchunguzi ambapo kwa Afrika nchi 20 ikiwemo nchi yetu zilishiriki.

Amesema kuwa ripoti hiyo inaonesha Tanzania Ina hali mbaya zaidi "kwa bahati mbaya Tanzania tangu mwaka 2019 uchunguzi inaonesha tupo kwenye hali mbaya tupo kwenye mstari mwekundu tunazidi kudidimia wakati wenzetu majirani zetu mfano Kenya, Uganda, Ethiopia, na mataifa mengine Afrika wanafanya vizuri sana"

Ameongeza kuwa utafiti huo umeangalia kanuni ya 5.3 ya mkataba wa kimataifa wa kudhibiti Tumbaku .

"Mkataba huu unazuia kwa nguvu zote kampuni za Tumbaku kuingilia sera za afya,"amesema.

Amesema kuwa matokeo hayo hayaridhishi "ombi letu moja kwa viongozi kwamba tunasheria mbovu iliyotungwa mwaka 2003 kabla mkataba wa Shirika la Afya duniani (WHO), haujaja ambapo ulitoka 2005 kwa hiyo hiyo sheria inamapungufu mengi lakini tulishatengeneza muswada unaoendana na mazingira"

Amesema kuwa muswada huo uliandaliwa kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wakiwemo WHO, Wizara ya Afya na wadau wengine "tangu 2017 ulikuwa upelekwe bungeni lakini mpaka leo ujapelekwa na tunaamini ni kwa sababu ya msukumo wa kampuni za Tumbaku,"

"Tunaiomba serikali huu muswada upelekwe bungeni haukatazi kulima Tumbaku au usiuze Tumbaku unaendelea kulinda afya za Watanzania na mazingira yao,"

Amesisitiza kuwa sheria hiyo itasaidia kudhibiti matumizi holela ya tumbaku "watu wasivute hovyo, mmeona shisha ilivyoonea usiwavutishe wengine kwa sababu kwa sasa hivi shisha sote ni wavutaji kama ukikaa pahala kunywa soda, kula chakula, utavuta shisha kwa hiyo tunaiomba serikali ipitishe huo muswada tupate sheria bora itakayoweza kulinda afya za Watanzania,". 

Naye, Daktari wa magonjwa ya ndani na mfumo wa upumuaji, Dkt. Mwanaada Kilima, amesema matumizi ya tumbaku yanaigharimu nchi zaidi kuliko faida inayopatikana.

“Kiasi cha kodi kinachopatikana kutokana na tumbaku ni takribani Sh bilioni 200 kwa mwaka, lakini gharama za matibabu ya madhara yake zinazidi Sh bilioni 800, hivyo ni wazi kuwa si biashara yenye faida bali inaleta hasara kubwa,” amesema.

Ameongeza kuwa mgonjwa mmoja wa magonjwa ya mfumo wa upumuaji anaweza kutumia zaidi ya Sh milioni nne kwa mwaka kwa matibabu, bila kujumlisha gharama za wagonjwa wa saratani na magonjwa ya moyo.

“Hii inaonesha mzigo mkubwa kwa taifa, na kama hatua hazitachukuliwa, gharama hizi zitaendelea kuongezeka na kuwa changamoto kubwa zaidi,” amesema.

Dkt. Kilima ametoa wito kwa vijana kuacha matumizi ya shisha na sigara, akisisitiza kuwa ni hatari kubwa kwa afya zao.





Babati, Manyara

‎‎Halmashauri ya Mji wa Babati mkoani Manyara ni miongoni mwa miji inayonufaika na utekelezaji wa mradi wa Uendelezaji wa Miundombinu ya Miji Tanzania (TACTIC) stendi mpya ya kisasa, barabara za lami pamoja na miradi mingine ya kijamii itajengwa kupitia mradi huo.

‎Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Babati, CPA. Shaaban Mpendu alibainisha hayo nakueleza kuwa wamepokea zaidi ya shilingi Bilioni 20.5 kwa ajili ya kujenga Stendi mpya ya kisasa ya mabasi itakayokuwa Stendi ya mkoa wa Manyara, barabara za katikati ya mji pamoja na mitaro ya maji ya mvua na maji taka kupitia mradi wa TACTIC.

‎ ‎"Baadhi ya barabara wakati wa mvua zimekuwa hazipitiki, mitaro imekuwa inafurika maji na kusababisha mafuriko, napenda kutoa shukrani zangu kwa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuweza kuiona changamoto hii na kuleta mradi huu utakaosaidia kuboresha shughuli za usafiri na usafishaji", alisema.

‎‎Aliongeza kuwa kupitia stendi hiyo ya kisasa uchumi utaimarika na ajira zitaongezeka kwani kutakuwa na vibanda vya kukatia tiketi, biashara, mama lishe na pia mapato yataongezeka kutoka shilingi milioni 40 kwa mwaka ambapo wanatarajia baada ya stendi kukamilika watakusanya zaidi ya shilingi milioni 250 kwa mwaka.

‎Naye, Mratibu wa mradi wa TACTIC Mhandisi Charles Ibengwe alisema kuwa fedha za mradi huo ni mkopo nafuu toka Benki ya Dunia huku mradi ukihusisha ujenzi wa stendi ya mabasi, ujenzi wa barabara ni Km 4.89, mifereji ya maji ya mvua Km 8.15 pamoja na ujenzi wa jengo la ofisi ya usimamizi wa mradi ambapo wanatarajia mradi utakamilika mwezi Oktoba 2026.

‎‎Kwa upande wake, Meneja wa TARURA wilaya ya Babati Mhandisi Aloyce Nombo alieleza kuwa kukamilika kwa barabara hizo kutaongeza mtandao wa barabara za lami hadi kufikia Km 18.9, ukilinganisha na Km 14.2 zilizokuwepo. Pia kutakuwa na ujenzi wa mifereji ya maji ya mvua katika kata ya Maisaka, Singe na Bagara itakayosaidia kuondoa adha ya maji yanayopita katika makazi ya watu na pia taa zikiwekwa wananchi watafanya kazi hadi usiku na taa hizo zitaimarisha usalama.

‎‎Naye, mkazi wa mtaa wa Gendikuu Bi. Sara Nzowa ameishukuru serikali kwa ujenzi wa mifereji kwani awali kipindi cha mvua maji yalikuwa yanaleta athari yanaingia ndani kwenye makazi ya watu, mifugo ilikufa ilienda na maji na mashamba yaliathirika lakini sasa ujenzi wa mifereji utasaidia kuondoa adha hiyo.‎

‎Vilevile, Bw. Issa Seif mkazi wa mtaa wa Babati ameishukuru serikali kwa matengenezo ya barabara za lami Babati mjini pindi zitakapokamilika barabara hizo zitasaidia kupendezesha mji na watafanya biashara bila wasiwasi huku taa zikiwekwa watafanya kazi hadi usiku na usalama utaongezeka.

‎Aidha, Bw. Abdulrahman Issa mkazi wa mtaa wa Sawe alisema kuwa tangu watangaziwe kutakuwa na ujenzi wa barabara ya lami katika eneo lao thamani ya ardhi imepanda na wapangaji wanaongezeka pia mradi ukikamilika uchumi wa wananchi wa maeneo hayo utaongezeka kwani barabara hiyo ni njia ya kuelekea barabara kuu ya Arusha.

‎‎Naye, Bw. Justin Majagi mkazi wa Babati ambaye amepata kazi katika ujenzi wa stendi ya mabasi ameishukuru serikali kwa mradi huo uliowasaidia vijana kama yeye kupata ajira inayomsaidia kuendesha maisha na kupata kipato.







NA VICTOR MASANGU, DAR

Maelfu ya wananchi mbali mbali wakiwemo viongozi wa serikali, viongozi wa dini, taasisi na mashirika binafsi ,mashabiki wa soka na mziki wa dansi pamoja na wananchi mbali mbali .... wamejitokeza kwa wingi katika makaburi ya Kinonddoni Jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kuhudhuria mazishi ya mfanyabiashara maarufu na mshabiki mkubwa wa klabu ya soka ya Simba Emmanuel Nderimo almaarufu Macha ambaye alifariki dunia machi 30 mwaka huu.

Katika mazishi hayo ambayo yalihudhuriwa na viongozi mbali mbali wa serikali pamoja na Chama Cha Mapinduzi (CCM),yaligubikwa na vilio na majonzi makubwa ambayo yalipelekea baadhi ya watu kushindwa kujizuia kwa kutokwa na machozi wakati wa kuuaga mwili huo.

Moja kati ya viongozi maarufu ambao walihudhuria msiba huo ni Mwenyekiti wa klabu ya soka ya Simba Murtaza Mangungu akiwa ameambtana na viongozi wengine mbali mbali wa klabu hiyo, ambapo amesema marehemu Emmanuel alikuwa na mchango mkubwa sana katika klabu hiyo kwani alikuwa mstari wa mbela katika kusaidia mambo mbali mbali

Pia Kamanda wa Polisi Kanda maalumu ya Dar es Salaam SACP Jumanne Muliro naye alikuwa ni mmoja wa viongozi wa ulinzi na usalama ambaye naye alifika kwa ajili ya kutoa heshima zake za mwisho kwa Marehemu Emmaanuel Nderimo.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Kibaha mjini Mhe,Silvestry Koka ambaye marehemu ni shemeji yake hakusita kumwelezea marehemu jinsi alivyokuwa ni mpambanaji katika mambo mbali nmbali na kwamba alikuwa ni mtu wa kusamehe sana pindi unapomkosea na kwamba alikuwa ni mstari wa mbele katika kutoa ushauri wenye kujenga.

"Kwa kweli mimi nimesimama hapa kwannza kabisa namshukuru mwenyezi Mungu muumba wa mbingu na nchi kwa kutukutanisha hapa katika msiba wa ndugu yetu Emmanuel lakini kitu ambacho nataka kukisema inapaswa tuishi kwa kupendana sana na ndio maana marehemu alikuwa na upendo mkubwa sana na watu mbali mbali na alikuwa ni mwepesi sana katika suala la kusamehe kwa hivyo inapaswa tujifunze mazuri ambayo ametuachia."amebainisha Mhe. Koka.

Nao baadhi ya viongozi na mashabiki akiwemo Mama Asha Baraka ambaye pia ni Mbunge wa viti maalumu kupitia tiketi ya chama cha mapinduzi (CCM) amesema kwamba ameguswa na kusikitishwa sana na msiba huo mzito kwani marehemu kwa upande wake alikuwa ni moja ya mtu muhimu sana katika kuleta chachu ya maendeleo katika ttimu pamoja na kuweza kusaidia mtu mmoja mmoja kwa hivyo ni pengo kubwa sana ambalo ameliacha.

Pia mwimbaji maarufu wa mziki wa dansi hapa nchini Ally Choki ni moja kati ya wasanii maarufu ambao walihudhulia katika msiba huo hadi kuweza kufika katika makaburi hayo ya Kinondoni kwa lengo la kumpumzisha ndugu yao na rafiki mkubwa wa burudani ya mziki wa dansi hapa nchini katika bendi mbali mbali.

Mazishi hayo ya marehemu Emmanule Nderimo ambayo yamefanyika katika makaburi ya Kinondoni Jijini Dar es Salaam yameweza kuhudhuliwa na umati wa maelfu ya watu kutoka sehemu mbali mbali wakiwemo viongozi wa serikali, viongozi wa chama, viongozi wa madhehebu ya dini, taaasisi wezeshi,wasanii maarufu, pamoja na wananchi ambao wamewza kufika na kumuhifadhi katika nyumba yake ya milele.







Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amewataka Watanzania kulinda, kuimarisha na kudumisha Muungano wa Tanzania, amani, utulivu na umoja wa kitaifa kama msingi wa maendeleo endelevu.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo tarehe 02 Aprili , 2026 wakati wa uzinduzi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026 uliofanyika Uwanja wa Gombani, Pemba.

Aidha, Rais Mwinyi amesema taasisi zote nchini na wananchi kwa ujumla wana wajibu wa kuheshimu utu, haki, usawa na utawala wa sheria ili kuendeleza mshikamano wa Taifa.

Ameeleza kuwa Mwenge wa Uhuru unaendelea kuwa chombo muhimu cha kuhamasisha uzalendo, uwajibikaji na mapambano dhidi ya maadui wa maendeleo wakiwemo umasikini, ujinga na maradhi.

 Vilevile, amewahimiza Watanzania kupinga ubaguzi wa aina yoyote na kuunga mkono juhudi za Serikali katika kupambana na rushwa, dawa za kulevya na magonjwa kama UKIMWI na malaria.

Halikadhalika,  Rais Dkt. Mwinyi amebainisha kuwa Serikali inaendelea kuimarisha huduma za afya, kudhibiti matumizi ya dawa za kulevya na kupunguza maambukizi ya malaria, huku akisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa wadau wote katika kufanikisha maendeleo ya Taifa.

Mwenge wa Uhuru umeanza mbio zake katika Mkoa wa Kusini Pemba na unatarajiwa kufikia kilele chake Oktoba 14, 2026 mkoani Rukwa, ukiwa na kaulimbiu: “Tanzania ni Yetu Sote, Tushikamane.”


















Top News