WANANCHI Watakiwa kujikita zaidi katika Kusoma na Kujifunza zaidi Elimu ya Usalama Barabarani ili kuepuka ajali zisizo za lazima hususani kwa Watoto Mashuleni.

Akizungumza na Wanahabari Jijini Dar es Salaam Mkurugenzi kutoka Chama cha  Mbio za Magari (AAT) Najma Rashid amesema kuwa Chama hicho kwa kushirikiana na  shirikisho la mbio za Magari duniani (FIA) kumekuwa na ushirikiano mzuri na wakaribu zaidi ili kuhakikisha programu ya mafunzo kwa ajili ya madereva pamoja na

watoto wa shule za sekondari na Misingi na wananufaika na Elimu ya Usalama barabarani ikiwemo kuzifahamu Alama za Barabarani, na Kuhakikisha wanarekebisha Miundombinu Barabarani (vivuko).

Hata hivyo amesema Mafunzo hayo yalianza mapema mwaka jana 2025 katika shule zilizopo Wilaya ya Kinondoni na hatimae kwa sasa ni Wilaya ya Ubongo na kusogea Wilaya ya Temeke Kwa Mwakani.

Pia ameeleza kuwa mwitikio umekuwa mkubwa zaidi kutokana na kupungua kwa ajali kwa watoto mashuleni na kwa Karibu wamekuwa wakipewa ushirikiano mkubwa na Askari wa Usalama Barabarani ambao ndio Wakufunzi katika Shule hizo.

Kwa Upande wa Mkufunzi wa programu hiyo ya Usalama Barabarani Askari sajenti Letcia Ishengoma kutokea traffic Makao Makuu amesema wamekuwa wakiendelea kutoa Elimu kila kona ikiwemo mashuleni,vijiwe vya bodaboda,stendi za mabasi ambapo tunatoa elimu ili watu waweze kubaini makosa kabla ya kutoa hukumu au adhabu ikiwemo faini na mengineyo pamoja na namna sahihi ya kutumia Alama za Barabarani.

Aidha amesema kuwa Jeshi la polisi litaendelea kutoa elimu ni Jambo endelevu ili kudhibiti tatizo mapema kabla ajali haijatokea hivyo programu hii inawanufaisha Wanafunzi Mashuleni ili kuwajengea uwezo wa kujua Alama za Barabarani na Kunusuru Ajali na vifo.




MKUTANO wa kikanda unaolenga kuimarisha mifumo ya tahadhari za mapema na huduma za hali ya hewa kwa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika umefunguliwa rasmi leo tarehe 13 Julai 2026 jijini Arusha.

Mkutano huu unawakutanisha wataalamu wa hali ya hewa na wadau kutoka nchi mbalimbali katika Bara la Afrika kujadili na kuweka mikakati ya kuimarisha utoaji wa tahadhari za matukio ya hali mbaya ya hewa na kuimarisha huduma za hali ya hewa kwa ujumla. Baadhi ya Nchi zinazo shiriki ni pamoja na Tanzania, Kenya, Misri, Angola, Madagascar, Afrika Kusini n.k.

Mkutano huo umeandaliwa kwa ushirikiano wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Ofisi ya Hali ya Hewa ya Uingereza (UK Met Office) na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA).

Katika hotuba yake ya ufunguzi, Dkt. Ladislaus Chang'a, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kitaifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa naTabianchi (IPCC), alisisitiza umuhimu wa kuimarisha usambazaji na uzingatiaji wa taarifa za utabiri na tahadhari. Vile vile, alibainisha kuwa, Mkutano wa 20 wa Baraza la Sekta ya Uchukuzi, Mawasiliano na Hali ya Hewa kwa Afrika Mashariki ulipitisha mapendekezo ya kuimarisha Taasisi za Kitaifa za Hali ya Hewa na kuchukua hatua stahiki ili kupunguza athari zinazoweza kusababishwa na El Nino 2026.

Kwa upande wake, Dkt. Agnes Kijazi, Mkurugenzi wa Ofisi ya Kanda ya Afrika ya WMO, alisisitiza kuwa hali ya hewa haina mipaka, na hivyo ushirikiano wa kimataifa ni muhimu sana. Alifafanua kuwa mkutano huo unalenga kuimarisha uratibu kati ya taasisi za kikanda ikiwemo Vituo Maalum vya Hali ya Hewa vya Kikanda ili kuongeza uwezo wao wa kusaidia Wanachama wa WMO katika kutoa huduma za hali ya hewa. "Hili ni jukumu kubwa ambalo haliwezi kutekelezwa bila kukuza ushirikiano wa kimataifa," alisisitiza Dkt. Kijazi.

Naye, Fionne Marshall, Kiongozi wa Kanda ya Afrika kutoka Ofisi ya Hali ya Hewa ya Uingereza, alitoa wito wa utabiri na tahadhari kuwa sahihi, zenye kuaminika, na zenye kutoa hatua stahiki zakuchukuliwa. "Haitoshi kujua kwamba mvua kubwa inakuja ikiwa watu hawaelewi athari kubwa zinaweza kutokea. "Haitoshi kutoa tahadhari ikiwa jamii hazipati, haziiamini, au hazijui hatua ya kuchukua," alisema Marshall, akiwataka taasisi kufanya kazi kwa mwelekeo mmoja wa kuelewa athari.

Wawakilishi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Kamisheni ya Umoja wa Afrika (AUC) walithibitisha majukumu yao katika kuimarisha mifumo ya tahadhari za mapema, huku James Kivuva wa EAC akibainisha kuwa uratibu bado ni pengo muhimu ambalo lazima lifanyiwe kazi na lifungwe. Naye, Dkt. Jolly Wasambo wa AUC alisisitiza dhamira ya bara kama ilivyoainishwa katika Agenda 2063, akisisitiza kwamba hali ya joto duniani inavyoendelea kuongezeka ndivyo ulazima wa kuimarisha mifumo ya tahadhari mapema unavyohitajika kwaajili ya jamii salama.

Kuanzia tarehe 13 hadi 17, washiriki watajadili namna ya kuimarisha vituo vya kikanda, kuimarisha Taasisi za Kitaifa za Hali ya Hewa, kuimarisha utabiri unaozingatia athari kwa ajili ya El Nino 2026, na kuimarisha ushirikiano katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT) na Akili Unde.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali itaendelea kuimarisha ushirikiano na Benki ya CRDB katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya maendeleo Zanzibar.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 14 Julai 2026, alipokutana na uongozi pamoja na wajumbe wa Bodi ya Benki ya CRDB, waliofika Ikulu Zanzibar kwa mazungumzo.

Amesema Serikali inathamini mchango wa benki hiyo katika kufanikisha miradi mbalimbali ya maendeleo na itaendelea kufanya kazi kwa karibu katika ujenzi wa skuli, nyumba za makaazi, miradi ya kilimo na kuwezesha upatikanaji wa mikopo kwa wananchi.

Aidha, ameipongeza CRDB kwa kutoa mikopo kwa wajasiriamali wadogo na wa kati, kuwajengea uwezo watendaji wa sekta ya umma na kuisaidia Serikali kupata mikopo kutoka taasisi za fedha za kimataifa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya CRDB, Prof. Neema Munisi Mori, amesema benki hiyo itaendelea kushirikiana na Serikali katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo na programu za kuwawezesha vijana, wanawake na wajasiriamali.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB, Dkt. Abdulmajid Mussa Nsekela, ameipongeza Serikali kwa maendeleo yaliyofikiwa na kuanzishwa kwa akaunti maalum ya kulipa madeni ya mikopo ya miradi ya kimkakati, hatua iliyoongeza ufanisi na kuimarisha imani ya taasisi za fedha kwa Serikali.
















Balozi wa Tanzania nchini China, Dkt. Suleiman Haji, akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo Julai 14, 2026.
Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA), Gilead Teri akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo Julai 14, 2026.

Na Mwandishi Wetu
WAKATI uhusiano wa kibiashara kati ya Tanzania na China ukiendelea kuimarika, Balozi wa Tanzania nchini China, Dkt. Suleiman Haji, amesema tathmini ya ushiriki wa Ubalozi wa Tanzania katika Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) imeibua mkakati wa kuwasaidia Watanzania kutumia fursa za biashara na uwekezaji katika soko la China.

Akizungumza na waandishi wa habari leo, Julai 14, 2026, Dkt. Haji alisema takribani Watanzania 500 walitembelea banda la ubalozi huo na kubaini changamoto mbalimbali zinazowakabili wafanyabiashara wanaotaka kufanya biashara za kimataifa.

Alisema changamoto hizo ni pamoja na uzalishaji hafifu usiokidhi viwango vya kimataifa, uelewa mdogo wa taratibu za biashara za kimataifa, pamoja na udhaifu wa vifungashio unaopunguza ushindani na thamani ya bidhaa za Tanzania katika masoko ya nje.

Aidha, alisema wafanyabiashara wengi walieleza kuwa baadhi ya taasisi zinazopaswa kuwawezesha kushiriki katika biashara za kimataifa zimekuwa zikikwamisha juhudi zao badala ya kuzisaidia.

Dkt. Haji alisema Tanzania ina fursa kubwa za kushirikiana na China katika sekta za kilimo, uvuvi, nishati na madini, huku akibainisha kuwa idadi ya watalii kutoka China wanaotembelea Tanzania imefikia takribani 82,000 na inatarajiwa kufikia 100,000 mwaka ujao.

Kutokana na changamoto zilizobainika, alipendekeza kuanzishwa kwa Kliniki ya Biashara itakayotoa elimu na ushauri kuhusu biashara za kimataifa, kuboreshwa kwa utekelezaji wa sera ya ushuru sifuri, kuimarishwa kwa elimu kuhusu fursa zilizopo China na masoko mengine, pamoja na kuanzishwa kwa kituo kimoja kitakachounganisha taasisi zote zinazoshughulikia biashara za kimataifa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA), Gilead Teri, alimpongeza Dk. Haji kwa kuanzisha zoezi hilo, akisema litakuwa na mchango mkubwa katika kuongeza ushiriki wa Watanzania katika biashara za kimataifa na kuvutia uwekezaji nchini.




Na Mwandishi Wetu
MAMLAKA ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) imeibuka mshindi wa kwanza katika kundi la Taasisi za Udhibiti kutokana na utoaji bora wa elimu kwa wananchi katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) 2026.

Akizungumza mara baada ya kupokea tuzo hiyo, Meneja wa PPRA Kanda ya Pwani, Vicky Mollel, alisema ushindi huo ni heshima kubwa kwa mamlaka hiyo na umetokana na imani na ushirikiano mkubwa waliooneshwa na Watanzania waliotembelea banda la PPRA wakati wa maonesho hayo.

Alisema PPRA itaendelea kuboresha huduma zake ili kuhakikisha wananchi wanapata elimu na huduma za ununuzi wa umma kwa viwango vya juu, sambamba na kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa.

"Ushindi huu ni heshima kwa PPRA na unatupa nguvu ya kuendelea kuwahudumia Watanzania kwa ufanisi zaidi. Tunaendelea kujizatiti kuhakikisha huduma zetu zinabaki kuwa bora wakati wote," alisema Mollel.

Alibainisha kuwa katika kipindi chote cha maonesho, wananchi wengi walifika kwenye banda la PPRA kupata elimu kuhusu mfumo wa kielektroniki wa ununuzi wa umma (NeST), huku idadi kubwa wakijisajili ili kushiriki katika zabuni na fursa mbalimbali za ununuzi wa umma.

Mollel alisema mwitikio huo unaonesha kuongezeka kwa uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa kushiriki katika ununuzi wa umma kwa kutumia mifumo ya kidijitali, jambo linalochangia uwazi, ushindani na uwajibikaji katika matumizi ya fedha za umma.

Alisisitiza kuwa PPRA itaendelea kutoa elimu kwa wadau na wananchi nchini kote ili kuongeza ushiriki wa Watanzania katika fursa za ununuzi wa umma, huku ikihakikisha shughuli zote zinaendeshwa kwa kuzingatia sheria na taratibu zinazotawala sekta hiyo.
-Yatangaza Kampeni ya Kitaifa Kuhusu Elimu ya Uwekezaji wa Kustaafu.

Mfuko mpya wa uwekezaji wa kustaafu wa Foresight Private Retirement Fund (FPRF) umesisitiza dhamira yake ya kuleta mapinduzi katika mfumo wa uwekezaji wa kustaafu nchini kwa kuwapa Watanzania fursa ya kujenga uhuru wa kifedha kupitia uwekezaji wa hiari, salama na unaosimamiwa kitaalamu, huku ikitangaza kuanza kwa kampeni kubwa ya kitaifa ya elimu ya fedha itakayowafikia wadau mbalimbali nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo, Afisa Mtendaji Mkuu wa CORE Securities Limited, wasimamizi wa FPRF, CPA George Fumbuka, alisema kampeni hiyo ni hatua inayofuata baada ya uzinduzi rasmi wa mfuko huo na inalenga kujenga uelewa mpana kuhusu umuhimu wa kuwekeza mapema kwa ajili ya maisha ya baada ya kustaafu.

Alisema FPRF imeanzishwa kama suluhisho la muda mrefu litakalowasaidia Watanzania kujenga utajiri endelevu, kupunguza utegemezi wanapostaafu na kuimarisha ustawi wa familia zao.

"Tunataka kuanzisha utamaduni mpya wa kifedha nchini. Kwa muda mrefu watu wamekuwa wakifikiria kustaafu pale wanapokaribia kuacha kazi. Sisi tunasema maandalizi ya maisha ya baada ya kustaafu yanapaswa kuanza mapema. Swali si kama utastaafu, bali utaishije baada ya kustaafu. Ndiyo maana tunawahamasisha Watanzania waanze kuwekeza leo ili waishi kwa uhuru kesho," alisema CPA Fumbuka.

Alisema kwa miongo kadhaa mifumo ya pensheni imeonekana zaidi kuwa ya watu walio katika ajira rasmi, hali iliyosababisha mamilioni ya Watanzania wanaofanya kazi katika sekta isiyo rasmi kukosa fursa ya kujenga akiba na uwekezaji wa muda mrefu kwa ajili ya maisha yao ya baadaye.

Kwa mujibu wa CPA Fumbuka, FPRF imekuja kuziba pengo hilo kwa kutoa jukwaa linalowakaribisha Watanzania wote bila kujali aina ya shughuli wanazofanya, wakiwemo waajiriwa wa sekta ya umma na binafsi, wafanyabiashara, wakulima, wavuvi, wajasiriamali, vikundi vya kijamii, SACCOS, kampuni na taasisi mbalimbali.

Alieleza kuwa kampeni ya elimu itafanyika kupitia warsha, semina, mikutano ya wadau na majukwaa mbalimbali ya elimu ya fedha, kwa lengo la kuwawezesha wananchi kuelewa misingi ya uwekezaji wa kustaafu, namna ya kujiunga na mfuko huo, faida za kuwekeza kwa muda mrefu pamoja na mbinu bora za kupanga maisha ya kifedha baada ya kustaafu.

"Mafanikio ya FPRF hayatapimwa kwa idadi ya wanachama pekee, bali kwa kiwango cha uelewa tutakachojenga kwa Watanzania kuhusu umuhimu wa kupanga maisha yao ya baadaye. Elimu ndiyo msingi wa mkakati wetu. Tutawafuata wananchi walipo na kuwapa maarifa yatakayowasaidia kufanya maamuzi sahihi ya kifedha," alisema.

CPA Fumbuka alisisitiza kuwa FPRF haijaanzishwa kuchukua nafasi ya mifuko ya hifadhi ya jamii iliyopo, bali kuikamilisha kwa kutoa fursa za ziada za uwekezaji zitakazoongeza uwezo wa wananchi kujenga kipato na utajiri wa muda mrefu baada ya kustaafu.

"Tofauti na mifuko mingine inayojikita zaidi kwenye michango ya lazima, FPRF imejengwa katika misingi ya uchaguzi wa hiari, unyumbufu wa uwekezaji na uhuru wa mwananchi kupanga mustakabali wake wa kifedha kulingana na malengo na uwezo wake," alifafanua.

Aliongeza kuwa moja ya sifa kuu za FPRF ni kumpa mwekezaji uhuru wa kuchagua namna ya kunufaika na uwekezaji wake baada ya kutimiza masharti ya mfuko.

"Mwekezaji anaweza kuchagua kupokea mafao yake kwa mkupuo, kwa malipo ya kila mwezi kama pensheni au kwa mchanganyiko wa njia hizo kulingana na mahitaji yake. Vilevile anaweza kuanza kwa kiwango anachomudu na kuongeza uwekezaji wake kadri uwezo wake wa kifedha unavyoongezeka," alisema.

Kwa upande wake, Meneja wa Mfuko wa FPRF, Bw. Richard Matekele, alisema mfuko huo umeandaliwa kwa kuzingatia mahitaji tofauti ya wawekezaji kupitia mipango mitatu ya uwekezaji inayozingatia umri na malengo ya kifedha ya mwanachama inayofahamika kama Youngsters' Plan, Middle-Agers' Plan na Seniors' Plan

“Youngsters' Plan inalenga vijana walio chini ya miaka 35 kwa lengo la kukuza mtaji kwa kipindi kirefu, Middle-Agers' Plan imeundwa kwa watu wenye umri wa miaka 35 hadi 50 wanaohitaji uwiano kati ya ukuaji wa uwekezaji na usalama wa mtaji, huku Seniors' Plan ikiwalenga wawekezaji wenye zaidi ya miaka 50 kwa kuzingatia zaidi uhifadhi wa mtaji na upatikanaji wa mapato yenye uhakika.’’ Alitaja.

Bw. Matekele alibainisha kuwa wawekezaji wanaweza kuchangia kwa mkupuo au kwa michango ya kila mwezi kulingana na uwezo wao, huku fedha zao zikiwekezwa katika hisa, hati fungani, dhamana za Serikali na vyombo vingine vya masoko ya mitaji vinavyolenga kuongeza thamani ya uwekezaji kwa muda mrefu.

Akifafanua zaidi kuhusu kampeni hiyo, Bw Matekele alisema itawafikia waajiri, wafanyakazi, taasisi za elimu, vyama vya wafanyakazi, SACCOS, vikundi vya kijamii, wafanyabiashara, wajasiriamali, wakulima, wanawake na vijana ili kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa kuwekeza mapema kwa ajili ya maisha ya baada ya kustaafu.

"Kila hatua unayoanza leo ni uwekezaji katika heshima yako, familia yako na uhuru wako wa kifedha kesho. Usisubiri ustaafu ndipo uanze kupanga maisha ya baadaye. Anza Leo – Wekeza Kustaafu, Ishi kwa Uhuru Kesho” alisisitiza.

Foresight Private Retirement Fund (FPRF) ni mfuko wa uwekezaji wa kustaafu uliopata idhini ya Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) na unasimamiwa na CORE Securities Limited, huku mali za mfuko zikihifadhiwa na NMB Bank PLC kama Mdhamini na Mlezi (Trustee/Custodian). Mfuko huo umeanzishwa kwa lengo la kupanua fursa za uwekezaji wa muda mrefu na kuwasaidia Watanzania kujenga ustawi wa kifedha na maisha yenye heshima baada ya kustaafu.


Mtendaji Mkuu wa CORE Securities Limited, wasimamizi wa Mfuko mpya wa uwekezaji wa kustaafu wa FPRF, CPA George Fumbuka (kulia) akifafanua jambo mbele ya waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati akizungumza kuhusu mapokeo ya wadau kwa mfuko huo sambamba na ujio wa kampeni ya kitaifa inayolenga kujenga uelewa mpana kuhusu umuhimu wa kuwekeza mapema kwa ajili ya maisha ya baada ya kustaafu. Mkutano huo umefanyika leo jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Meneja wa Mfuko wa FPRF, Bw. Richard Matekele


Meneja wa Mfuko mpya wa uwekezaji wa kustaafu wa FPRF, Bw. Richard Matekele (kushoto) akifafanua jambo mbele ya waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati akizungumza kuhusu mapokeo ya wadau kwa mfuko huo sambamba na ujio wa kampeni ya kitaifa inayolenga kujenga uelewa mpana kuhusu umuhimu wa kuwekeza mapema kwa ajili ya maisha ya baada ya kustaafu. Mkutano huo umefanyika leo jijini Dar es Salaam. Kulia ni Mtendaji Mkuu wa CORE Securities Limited, wasimamizi wa Mfuko mpya wa uwekezaji wa kustaafu wa FPRF, CPA George Fumbuka.
NA DENIS MLOWE,IRINGA

MBUNGE wa Jimbo la Iringa Mjini, Fadhili Ngajilo, amekabidhi msaada wa vifaa mbalimbali vya elimu kwa watoto wenye maisha duni wanaosoma katika shule za msingi mkoani Iringa, akisisitiza wazazi kuhakikisha watoto wote, wakiwemo wenye ulemavu, wanapata haki yao ya elimu.

Akizungumza katika hafla iliyofanyika katika Shule ya Msingi Ugele, Ngajilo alikabidhi magodoro, madaftari, mahindi, maharage, matranka na vifaa vingine muhimu vinavyolenga kuboresha mazingira ya kujifunzia na kuishi kwa watoto hao.

Ngajilo aliwataka wazazi kuacha tabia ya kuwaficha watoto wenye ulemavu majumbani, akisema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imejipanga kuhakikisha kila mtoto anapata fursa ya elimu bila ubaguzi.

Alisema watoto wenye ulemavu wana uwezo mkubwa wa kufanikiwa iwapo watapata elimu na malezi bora, akitoa mfano wa watu wenye ulemavu waliofanikiwa duniani na nchini, wakiwemo wabunge wanaowakilisha wananchi bungeni.

"Ninawasihi wazazi, msiwafiche watoto wenye ulemavu wapeleke shule kwa sababu huwezi kujua atakuwa nani kesho. Elimu ndiyo msingi wa mafanikio yao," alisema Ngajilo.

Aliwapongeza walimu wanaofundisha watoto hao kwa kujitolea na kuendelea kutekeleza majukumu yao licha ya changamoto mbalimbali zinazowakabili, akisema kazi yao ni wito unaohitaji moyo wa upendo na uvumilivu.

Ngajulo alieleza kuwa jukumu la viongozi ni kuweka mazingira bora ya watoto kupata elimu na huduma muhimu, huku akisisitiza kuwa malezi bora yanahitaji ushirikiano wa karibu kati ya wazazi na walimu.

Aliwataka wazazi kufuatilia maendeleo ya watoto wao hata wanaporudi nyumbani kwa kuwasaidia kufanya kazi za nyumbani (homework) ili kuongeza ufanisi katika kujifunza.

Ngajilo aliongeza kuwa ana matumaini kuwa kupitia uwekezaji katika elimu, Mkoa wa Iringa utaendelea kuzalisha wataalamu mbalimbali wakiwemo madaktari, wahandisi, maprofesa na viongozi watakaochangia maendeleo ya taifa.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi wa serikali, walimu, wazazi na wanafunzi, huku msaada huo ukitarajiwa kusaidia kuboresha ustawi wa watoto wenye maisha duni na kuongeza fursa zao za kupata elimu bora.





NA DENIS MLOWE- MUFINDI, IRINGA

KAMATI ya Siasa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Iringa ikiongozwa na Mwenyekiti wake, Daudi Yassin, imetembelea na kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 23.6 katika Wilaya ya Mufindi, ikiwemo barabara ya kiwango cha lami ya Mtiri–Ifwagi pamoja na mtambo wa kuzalisha oksijeni tiba katika Hospitali ya Mji Mafinga.

Mradi mkubwa wa barabara ya Mtiri–Ifwagi wenye urefu wa kilomita 14 umegharimu shilingi bilioni 21.9, huku mradi wa mtambo wa kuzalisha oksijeni tiba katika Hospitali ya Mji Mafinga ukigharimu shilingi bilioni 1.78, fedha zilizotolewa kupitia Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ushirikiano na washirika wa maendeleo.

Akiwasilisha taarifa ya mradi wa barabara, kwa. Kamati ya Siasa,Meneja wa Tarura Mkoa wa Iringa Injinia Davies Tembo alisema kuwa barabara hiyo ilijengwa chini ya Mradi wa RISE (Roads to Inclusion and Socioeconomic Opportunities), unaofadhiliwa na Benki ya Dunia kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania, kupitia Ofisi ya Rais-TAMISEMI na Wizara ya Ujenzi.

Alisema kuwa mradi huo ulianza Julai 27, 2023 na kukamilika Desemba 28, 2024, huku kipindi cha uangalizi wa mkandarasi (Defects Liability Period) kikimalizika Juni 30 mwaka huu.


Injinia Tembo alisema kuwa ujenzi wa barabara umehusisha kukata milima, kupasua miamba, kujenga madaraja mawili, makalavati 37, kuweka tabaka mbalimbali za barabara pamoja na kufunga taa za barabarani 90.

Aidha, maeneo yenye miteremko mikali yalijengwa kwa zege ili kuongeza uimara wa miundombinu hiyo na kukamilika kwa barabara hiyo kumerahisisha usafirishaji wa mazao ya misitu, chai, mboga mboga na mazao mengine ya biashara, kupunguza gharama za usafiri, pamoja na kuboresha upatikanaji wa huduma za kijamii ikiwemo afya, elimu na huduma za kiutawala kwa wananchi wa Ifwagi na maeneo jirani.

Kamati hiyo pia ilikagua mradi wa mtambo wa kuzalisha oksijeni tiba katika Hospitali ya Mji Mafinga uliotekelezwa kwa gharama ya shilingi bilioni 1,781,750,519.23 kupitia fedha za Serikali Kuu na Global Fund.

Mganga Mkuu wa halmashauri ya Mji Mafinga Dkt Bonaventula Chitopela akieleelezea kuwa mtambo huo una uwezo wa kuzalisha mitungi 60 ya oksijeni yenye ujazo wa lita 100 kwa siku na umeongeza kwa kiwango kikubwa ubora wa huduma za afya kwa wagonjwa wa dharura, wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalumu (ICU), watoto wachanga pamoja na wajawazito.
Aidha, ulieleza kuwa kabla ya uwepo wa mtambo huo hospitali ilikuwa ikitumia wastani wa shilingi milioni tisa kununua oksijeni, lakini gharama hizo zimepungua hadi kufikia milioni nne kwa mwezi, hali inayookoa takribani shilingi milioni tano kila mwezi.

Hospitali hiyo pia imekuwa ikisambaza oksijeni tiba katika Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi, Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Iringa, Hospitali ya Manispaa ya Iringa, Hospitali ya Ipamba pamoja na vituo vingine vya kutolea huduma za afya.

Akizungumza baada ya kukagua miradi hiyo, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Iringa, Daudi Yassin, alisema Kamati ya Siasa imeridhishwa na ubora wa utekelezaji wa miradi hiyo kwani imeleta matokeo chanya kwa wananchi.

Alisema mradi wa mtambo wa oksijeni umeondoa changamoto ya upatikanaji wa huduma za dharura na kupunguza gharama za matibabu, huku barabara ya Mtiri–Ifwagi ikiwa imefungua fursa mpya za kiuchumi kwa wakazi wa Mufindi.

Yassin aliwataka wananchi kuendelea kuitunza miundombinu hiyo ili iweze kudumu na kuendelea kutoa manufaa kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

Alisema utekelezaji wa miradi hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya CCM na kwamba wananchi wa Mufindi ni mashahidi wa ahadi zilizotekelezwa na serikali.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Ifwagi, Arafat Benson Mwambule, alimshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kupeleka fedha za ujenzi wa barabara hiyo, akisema tayari imeanza kuleta mabadiliko makubwa ya maendeleo katika eneo hilo na kwamba wananchi wana matarajio makubwa ya kuendelea kwa ujenzi wa kilomita nyingine zilizopangwa.

Naye Mwenyekiti wa Kijiji cha Ifwagi, Fransis Bilangulo, alisema barabara hiyo imebadilisha sura ya kijiji na kuongeza shughuli za maendeleo, akieleza kuwa wananchi wanaiona Ifwagi kuwa miongoni mwa maeneo yaliyonufaika zaidi na uwekezaji wa serikali katika miundombinu.

Ziara hiyo ya Kamati ya Siasa ya CCM Mkoa wa Iringa ni sehemu ya ukaguzi wa utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi pamoja na kutathmini maendeleo ya miradi inayotekelezwa na Serikali katika Wilaya ya Mufindi na itaendelea kesho kwa wilaya ya Iringa.




 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ameishukuru Serikali ya Sweden kwa ushirikiano wake wa muda mrefu katika kuchangia maendeleo ya Zanzibar, huku akisisitiza umuhimu wa kuimarisha zaidi uhusiano wa pande hizo mbili kupitia biashara na uwekezaji.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 14 Julai 2026, alipokutana na Balozi wa Sweden nchini Tanzania, Mhe. Charlotta Ozaki Macias, aliyefika Ikulu Zanzibar kwa ajili ya kumuaga baada ya kumaliza muda wake wa kazi nchini.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeendelea kuweka mazingira rafiki na ya kuvutia uwekezaji katika sekta mbalimbali za kiuchumi, hususan nishati, uchumi wa buluu na kilimo cha mwani.

Ameeleza kuwa Serikali inakaribisha makampuni kutoka Sweden kuwekeza Zanzibar, hasa katika uzalishaji wa nishati mbadala ili kuongeza uzalishaji wa umeme na kuimarisha maendeleo ya uchumi.

Halikadhalika, Rais Dkt. Mwinyi amesema Serikali imejipanga kuongeza thamani ya zao la mwani kwa kulisindika na kuzalisha bidhaa mbalimbali, hatua itakayoongeza kipato cha wakulima na kuchochea ukuaji wa uchumi wa buluu.

Vilevile Rais Dkt.Mwinyi amesisitiza kuwa Zanzibar inaendelea kuthamini mchango wa Sweden katika sekta za elimu, afya na ustawi wa jamii, huku akiiomba nchi hiyo kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Zanzibar 2050.

Kwa upande wake, Balozi wa Sweden nchini Tanzania, Mhe. Charlotta Ozaki Macias, amempongeza Rais Dkt. Mwinyi na wananchi wa Zanzibar kwa hatua muhimu ya kuimarisha maridhiano ya kisiasa kupitia Tamko la Pamoja na utiaji saini wa Ajenda za Kuchukuliwa Hatua kati ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo.








 


Mkuu wa Idara ya Masoko na Uwezeshaji, Vodacom Tanzania Plc, Joseph Sayi (kulia) na Mkuu wa Kanda ya Dar es Salaam na Pwani wa kampuni hiyo Happiness Shuma (kushoto), wakiwa wameshika tuzo zilizotolewa kwa Vodacom Tanzania kutambua mchango wake katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam (SABASABA). Maonesho hayo yaliyofanyika Juni 28 hadi Julai 13, 2026, yaliipa Vodacom Tanzania fursa ya kuonyesha namna teknolojia inavyobadilisha maisha, kuwezesha huduma za kidijitali na kuimarisha nafasi yake kama kinara wa huduma za mawasiliano nchini.
Meneja Masoko wa Kanda ya Dar es Salaam na Pwani wa Vodacom Tanzania Plc, Caleb Majo (kushoto), akitoa elimu kuhusu huduma zinazotolewa na Vodacom Tanzania wakati wa mahojiano maalumu na Azam Media katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam (SABASABA). Maonesho hayo yaliyofanyika Juni 28 hadi Julai 13, 2026, yaliipa Vodacom Tanzania fursa ya kuonyesha namna teknolojia inavyobadilisha maisha, kuwezesha huduma za kidijitali na kuimarisha nafasi yake kama kinara wa huduma za mawasiliano nchini. Wengine ni Meneja Uhusiano wa Vodacom Tanzania Plc, Alex Bitekeye (wa pili kushoto), Mkuu wa Kanda ya Dar es Salaam na Pwani wa Vodacom Tanzania Plc, Happiness Shuma (wa pili kulia), na Mtangazaji wa Azam Media, Jafar Mponda (kulia).
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi (aliyekaa katikati), Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga (aliyekaa kushoto), na Mkurugenzi Mkuu wa TANTRADE, Latifa Khamis (aliyekaa kulia), wakiwa katika picha ya pamoja na wawakilishi wa kampuni mbalimbali, akiwemo Mkuu wa Kanda ya Dar es Salaam na Pwani wa Vodacom Tanzania Plc, Happiness Shuma (aliyevaa tisheti nyekundu), muda mfupi baada ya kufungwa kwa Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa Dar es Salaam (SABASABA). Vodacom Tanzania Plc ilitambuliwa kama mshirika muhimu wa maonesho hayo baada ya kupewa tuzo mbili; Tuzo ya Nafasi ya Tatu kwa Mshindi wa Jumla wa Maonesho na Tuzo ya Nafasi ya Pili ya Udhamini, ikiwa ni ishara ya kutambua mchango wake katika kufanikisha maonesho hayo.
Mkuu wa idara ya Masoko na Uwezeshaji wa Vodacom Tanzania Plc, Joseph Sayi (wa sita kulia), na Mkuu wa Kanda ya Dar es Salaam na Pwani wa kampuni hiyo Happiness Shuma (wa sita kushoto) wakiwa katika picha ya Pamoja na wafanyakazi wengine wa Vodacom wakiwa wa wameshika tuzo zilizotolewa kwa Vodacom Tanzania kutambua mchango wake katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam (SABASABA) muda mfupi baada ya kufungwa rasmi kwa maonesho hayo. Kwa siku zote 13 za maonesho hayo Vodacom Tanzania ilishiriki fursa ya kuonyesha namna teknolojia inavyobadilisha maisha, kuwezesha huduma za kidijitali na kuimarisha nafasi yake kama kinara wa huduma za mawasiliano nchini.

 Na Benny Mwaipaja, Horohoro, Tanga

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), ametoa wito kwa wafanyabiashara, wawekezaji na wazalishaji nchini kuongeza uzalishaji wenye tija na kuimarisha mauzo ya bidhaa katika masoko ya kimataifa ili kupunguza nakisi ya biashara (trade deficit) na kuongeza mchango wa sekta ya biashara katika kukuza uchumi wa Taifa.

Akizungumza wakati alipotembelea Kituo cha Huduma ya Pamoja Mpakani cha Horohoro, mkoani Tanga, ikiwa ni sehemu ya ziara yake mkoani humo, Mhe. Balozi Khamis alisema pamoja na mafanikio makubwa yaliyopatikana katika ukusanyaji wa mapato na uboreshaji wa mazingira ya biashara, bado ipo haja ya kuongeza thamani ya bidhaa zinazouzwa nje ya nchi ili Tanzania iweze kunufaika zaidi na biashara ya kimataifa.

Mhe. Balozi Omar alieleza kuwa takwimu za biashara kupitia Kituo cha Forodha cha Horohoro zinaonesha kuwa katika mwaka wa fedha uliopita bidhaa zenye thamani ya takribani shilingi bilioni 748 zilipitia katika kituo hicho, lakini kati ya hizo, bidhaa zilizouzwa nje ya nchi zilikuwa na thamani ya takribani shilingi bilioni 238 pekee, wakati bidhaa zilizoingizwa nchini zilifikia thamani ya shilingi bilioni 510, hali inayoonesha kuwepo kwa nakisi kubwa ya biashara.

"Matarajio ya kila taifa ni kuuza bidhaa nyingi zaidi kuliko linazoagiza kutoka nje, Takwimu hizi zinatuonesha bado tuna kazi kubwa ya kufanya katika kuongeza uzalishaji na kuimarisha mauzo ya bidhaa zetu nje ya nchi na Tanga ina fursa nyingi za uzalishaji na usafirishaji wa bidhaa, hivyo ni muhimu kuzitumia kikamilifu ili kupunguza nakisi hii," alisema Mhe. Balozi Khamis.

Alisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya biashara kupitia uwekezaji katika miundombinu ya forodha, mifumo ya kisasa ya ukaguzi wa mizigo pamoja na kuimarisha vituo vya mipakani ili kurahisisha biashara na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Aidha, alisema mafanikio ya ukuaji wa uchumi yanatoa msingi mzuri wa kuongezeka kwa shughuli za biashara nchini, akibainisha kuwa uchumi wa Tanzania ulikua kwa asilimia 5.9 mwaka 2025 na unatarajiwa kukua kwa asilimia 6.3 mwaka 2026, jambo litakalochochea ongezeko la uzalishaji na biashara.

Kwa upande wa ukusanyaji wa mapato, Mhe. Balozi Khamis alisema Kituo cha Huduma ya Pamoja Mpakani cha Horohoro, kimewekewa lengo la kukusanya shilingi bilioni 136 katika mwaka wa fedha 2026/27, baada ya kuvuka matarajio ya mwaka uliopita kwa kukusanya shilingi bilioni 125, hivyo kutokana na mwenendo mzuri wa ukuaji wa uchumi na biashara, Serikali ina imani kuwa lengo hilo litafikiwa, huku akibainisha kuwa kituo hicho kinachangia karibu robo ya mapato yote yaliyopangwa kukusanywa katika Mkoa wa Tanga.

“Serikali imetenga shilingi bilioni 573 katika Bajeti ya mwaka 2026/27 kwa ajili ya kuendeleza maboresho ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), ikiwemo ununuzi wa scanners (midaki) 27 za kisasa zitakazowekwa katika vituo mbalimbali vya forodha nchini, ikiwemo Kituo cha Forodha cha Horohoro” alisema Mhe. Balozi Omar

Alieleza kuwa mchakato wa ununuzi wa vifaa hivyo tayari umeanza na unafanyika kwa kuzingatia taratibu zote za ununuzi wa umma, huku akieleza kuwa vifaa hivyo hutengenezwa kwa kuzingatia mahitaji maalumu ya kila kituo cha forodha, hivyo mchakato wake unahusisha usanifu, utengenezaji, ukaguzi wa ubora, usafirishaji na ufungaji kabla ya kuanza kutumika na uwekezaji huo utaongeza ufanisi wa ukaguzi wa mizigo, kuharakisha utoaji wa huduma, kuimarisha usalama wa mipaka na kuongeza usahihi katika ukusanyaji wa mapato ya Serikali.

"Hatununui tu vifaa vya kisasa, bali tunawekeza katika kuongeza ufanisi wa biashara, kuimarisha usalama wa nchi na kuhakikisha Serikali inapata mapato yake stahiki, ma Midaki hii itasaidia kujua kwa uhakika bidhaa zinazopita mipakani, kupunguza muda wa ukaguzi na kurahisisha biashara halali," aliongeza Mhe. Balozi Omar.

Aliwahimiza pia wafanyabiashara kuendelea kutumia Kituo cha Huduma ya Pamoja Mpakani cha Horohoro, kufanya biashara halali na kuongeza mauzo ya bidhaa za Tanzania katika masoko ya nje, akisisitiza kuwa hatua hiyo itaongeza mapato ya fedha za kigeni, kupunguza nakisi ya biashara (trade deficit) na kuimarisha uchumi wa nchi.

Naye Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Tanga ambaye pia ni  Mkuu wa Wilaya ya Tanga mjini, Mhe. Dadi Kolimba, alisema Mkoa wa Tanga unaendelea kuwa miongoni mwa mikoa inayoongoza nchini katika ukusanyaji wa mapato, ukiwa wa sita kitaifa, mafanikio ambayo yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na utendaji mzuri wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) pamoja na ushirikiano wa taasisi nyingine za Serikali zinazofanya kazi katika vituo vya mipakani.

Alisema Kituo cha Forodha cha Horohoro ni miongoni mwa vituo muhimu vya kiuchumi vinavyochangia kwa kiwango kikubwa mapato ya Mkoa wa Tanga na Taifa kwa ujumla, akibainisha kuwa katika mwaka wa fedha uliopita kituo hicho kilivuka lengo lake kwa kukusanya shilingi bilioni 125 dhidi ya lengo la shilingi bilioni 115. Aliongeza kuwa Serikali ya Mkoa itaendelea kushirikiana na TRA kutatua changamoto zinazojitokeza, kuimarisha mazingira ya biashara na kuhamasisha uzalishaji pamoja na mauzo ya bidhaa za Tanzania katika masoko ya nje ili kuongeza mapato ya Serikali na kuchochea ukuaji wa uchumi.

Kwa Upande wao Naibu Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bw. Mcha Hassan Mcha, na Afisa Mfawidhi wa Kituo cha Huduma ya Pamoja Mpakani cha Horohoro, Bw. Shadrack Mbonea, walisema kuwa wamejipanga vyema kupambana na Magendo kwa kuimarisha doria za kimkakati kwa kushirikiana na taasisi nyingine za Serikali.

Walibainisha kuwa wataendelea kuimarisha ukaguzi wa mizigo inayoingia na kutoka nchini ili kuhakikisha wanatokomeza magendo lakini pia kuihakikisha kodi stahiki inakusanywa.

Katika Ziara hiyo Mhe. Balozi Omar aliambatana pia na, Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha ambaye pia ni Mhasibu Mkuu wa Serikali, CPA Leonard Mkude, Makamishna na maafisa waandamizi kutoka Wizara ya Fedha pamoja na taasisi zake.











Top News