Na Janeth Raphael – Michuzi TV

Watu wanane wamefariki dunia na wengine 66 kujeruhiwa kufuatia ajali mbaya iliyohusisha mabasi mawili ya abiria yaliyogongana uso kwa uso katika eneo la Ibihwa, Halmashauri ya Wilaya ya Bahi, mkoani Dodoma.

Kaimu Kamanda wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, Rehema Jeremia, amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo, akieleza kuwa ilihusisha basi la Isamilo lenye namba za usajili T 428 EXP, lililokuwa likitoka Mwanza kuelekea Dar es Salaam, na basi la Libanika Luxury lenye namba za usajili T 897 DUP, lililokuwa likitoka Dar es Salaam kuelekea Mwanza.

Akizungumza baada ya kuwatembelea majeruhi waliolazwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, amesema watu saba walifariki dunia papo hapo eneo la tukio, huku mtu mmoja akifariki baadaye alipokuwa akipatiwa matibabu hospitalini, na kufanya idadi ya vifo kufikia wanane.

Senyamule amesema kati ya majeruhi 66, watu tisa wanaendelea kupatiwa matibabu wakiwa katika hali mbaya, huku majeruhi 57 wakiwa katika hali ya kuridhisha.

Ameongeza kuwa majeruhi wamepelekwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma, Hospitali ya Makole na Hospitali ya Wilaya ya Bahi, ambako wanaendelea kupatiwa huduma za matibabu.

Kwa mujibu wa uchunguzi wa awali, chanzo cha ajali hiyo kinadaiwa kuwa ni dereva mmoja kujaribu kulipita gari lingine bila kuchukua tahadhari stahiki, hali iliyosababisha mabasi hayo kugongana uso kwa uso.

Mmoja wa majeruhi wa ajali hiyo, Jail Martin, amesema tukio hilo lilitokea majira ya saa 12:00 asubuhi baada ya basi walilokuwa wakisafiria kuanza kuyumba kabla ya kugongana uso kwa uso na basi lililokuwa likitokea upande wa pili wa barabara.

Jeshi la Polisi pamoja na vyombo vingine vya uokoaji vinaendelea na uchunguzi wa kina kubaini chanzo halisi cha ajali hiyo huku juhudi za kuwahudumia majeruhi zikiendelea.





Na Mwandishi Wetu

MJUMBE wa Kamati ya Utekelezaji ya Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Taifa, Mariam Abdallah Ibrahim ambaye pia ni Mbunge wa Mkoa wa Pwani ametoa Sh.milioni moja kwa ajili ya Kusaidia kukamilisha Ujenzi wa nyumba ya Mtumishi wa Jumuiya hiyo wilayani Gairo mkoani Pwani.


Mbunge Mariam amekabidhi fedha hizo akiwa katika ziara ya kutembelea na kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa na vikundi vya wajasiriamali hasa walioko kwenye Jumuiya ya UWT .

Akiwa katika ziara hiyo alipata nafasi ya kukagua pia nyumba ya mtumishi wa Jumuiya ya UWT Wilaya ya Gairo ambapo amekabidhi mchango wake wq fedha Sh. milioni moja ili kusaidia kukamilisha ujenzi wa nyumba ya mtumishi huyo.

Akizungumza na wananchi na wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) amewashukuru wakazi wa Mkoa wa Morogoro kwa kukichagua Chama Cha Mapinduzi katika Uchaguzi Mkuu kwa kumpatia kura nyingi Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na kuwachagua wabunge na madiwani wa chama hicho.

Mbunge Mariam pia amewahimiza wanawake kujitokeza kwa wingi kugombea nafasi za uongozi ndani ya CCM, akieleza kuwa ushiriki wao katika nafasi za maamuzi ni muhimu katika kuimarisha maendeleo na kuendelea kutetea maslahi ya wanawake na jamii kwa ujumla.

Ziara hiyo ni sehemu ya juhudi za UWT Taifa za kufuatilia utekelezaji wa shughuli za jumuiya hiyo, kuhamasisha maendeleo ya wanawake, na kuimarisha ushiriki wao katika shughuli za kisiasa, kijamii na kiuchumi.












Na Seif Mangwangi, Michuzi TV Arusha

WATUMISHI wa Wakala wa Vipimo nchini (WMA), wametakiwa kuhakikisha wanapambana ipasavyo na wafanyabiashara wahuni ambao wamekuwa wakiharibu vipimo kwa lengo la kuwaibia wanunuzi na kujipatia faida kubwa.

Aidha watumishi hao wametakiwa kuwa wazalendo kwa nchi hususani kwa bidhaa ambazo zimekwisha fungwa na kusafirishwa nje ya nchi kwa kuwa wakipitisha vipimo vilivyoharibiwa huiharibia nchi ndani na nje ya nchi.

Agizo hilo limetolewa leo Agosti 2, 2026, na Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Dennis Lazaro Londo, katika ufunguzi wa baraza la 38 la wafanyakazi wa wakala wa vipimo nchini unaoendelea Jijini Arusha.

Londo amesema ni wakati wa wafanyakazi wa wakala wa vipimo kuwa wazalendo na kumuogopa Mungu ili kuwajengea imani Watanzania juu ya mashine za vipimo wanazozikagua na kuzipa ithibati.

" Itapendeza sana mtu akinunua bidhaa yake aridhike na kuwa na imani, ni wajibu wenu kuwa wazalendo na kuwajengea imani Watanzania, sio sawa mtu anaenda kununua bidhaa kwa ujazo fulani kumbe umeshapunguzwa kupitia kipimo kisichokuwa sahihi, nendeni mkapambane na wahuni wote wanaoharibu vipimo," amesema.

Amesema wanaosafirisha bidhaa nje ya nchi zikiwa pungufu wanaharibu taswira ya nchi na matokeo yake ni kupoteza uaminifu Kwa wateja na zaidi ni kuharibia vizazi vijavyo kwa kukosa masoko na hivyo kuikosesha nchi mapato.

Wakati huo huo Naibu Waziri Londo amewataka watumishi hao kutumia mpango mkakati wake mpya2027/2030 kuongeza uwajibikaji na kwamba watafakari nafasi ya mtumishi mmoja mmoja katika kudhibiti uhuni wa wafanyabiashara wachache.

Kamishna wa vipimo nchini, Alban Kihulla amesema kupitia mpango mkakati wake mpya wanaenda kuongeza imani kwa wananchi kupitia ukaguzi wa vipimo.

Aidha amesema wanaenda kushirikiana na sekta binafsi ili kuboresha utendaji wao wa kazi, kuboresha mazingira ya ofisi zao na kuboresha mpango wa mafunzo kwa watumishi.

Kihulla amesema kupitia mpango mkakati wa miaka mitano iliyopita wakala wa vipimo umeweza kuhakiki mizani milioni5.5 pamoja na kujenga ofisi 26 za wakala wa vipimo nchini.

Amesema changamoto kubwa wanayopambana nayo ni kuwepo kwa adhabu ndogo kwa wanaochakachua vipimo ambapo Kwa mujibu wa Sheria ya wakala wa vipimo sura namba 340 adhabu ni laki moja na isizidi milioni 20.




Na Benny Mwaipaja, DURBAN

Nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) zimeazimia kuharakisha mageuzi ya kiviwanda katika kanda, baada ya kuhitimisha Wiki ya Tisa ya Viwanda ya SADC (SIW 2026) iliyofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Durban, jimbo la KwaZulu-Natal, Afrika Kusini.

Zimesisitiza umuhimu wa kuimarisha minyororo ya thamani ya kikanda, kuharakisha uwekezaji wa kiviwanda, kutumia ubunifu na teknolojia mpya, pamoja na kuimarisha ushirikiano kati ya serikali na sekta binafsi.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Kituo cha Fedha na Ubia cha Jumuiya ya Maendeleo Kusini Mwa Afrika (SADC), Bw. Zwelibanzi Sapula, alisema kuwa katika tathmini yake, mkutano ulibaini kuwa Ukanda wa Kusini mwa Afrika una rasilimali nyingi za asili, wajasiriamali wengi wanaokua na fursa kubwa za soko, lakini sekta ya viwanda haijatoa mchango mkubwa katika kuongeza mnyororo wa thamani katika rasilimali hizo.

Wajumbe walisisitiza kuwa ujenzi wa minyororo ya thamani ya kikanda iliyounganishwa kupitia ushirikiano katika kilimo, madini, dawa, uzalishaji wa magari, nguo na kemikali, ni muhimu kuongeza uongezaji thamani na kuimarisha ushindani wa viwanda vya SADC.

Vilevile, mabadiliko ya kidijitali, uchumi wa kijani, matumizi ya akili mnemba na teknolojia nyingine mpya vinabadilisha kwa kasi mifumo ya uzalishaji duniani, hivyo kuhitaji uwekezaji wa haraka kwenye miundombinu ya kidijitali na ya kijani, mifumo ya ubunifu, tafiti na uhawilishaji wa teknolojia.

Kilimo kilitajwa kuendelea kuwa nguzo muhimu ya mapinduzi ya viwanda, huku ukiwa na haja ya kuimarisha minyororo ya kiviwanda ya kilimo na kupanua sekta ya uchakataji wa mazao ili kuboresha usalama wa chakula, kuongeza mauzo nje na kutengeneza ajira, hasa kwa wanawake na vijana.

Utajiri wa madini muhimu wa kanda hiyo pia ulitajwa kuwa fursa ya kipekee ya kuiweka upya Kanda ya Kusini mwa Afrika kwenye minyororo ya kimataifa ya viwanda, kwa kuachana na uuzaji wa malighafi na badala yake kuwekeza kwenye uchakataji, uongezaji thamani na uzalishaji wa ndani.

Wajumbe pia walisisitiza kuwa wajasiriamali wadogo na wa kati ndio uti wa mgongo wa uchumi wa kikanda, hivyo upatikanaji wao wa mitaji, teknolojia, masoko, viwango na huduma za maendeleo ya biashara lazima uboreshwe.

Ilielezwa pia kuwa maendeleo endelevu ya viwanda hayawezi kufikiwa na serikali pekee, bali yanahitaji ushirikiano imara kati ya serikali, sekta binafsi, taasisi za fedha za maendeleo, wasomi na washirika wa maendeleo.

Wajumbe walihitimisha kuwa mafanikio ya ajenda ya uviwandishaji Kusini mwa Afrika yatategemea dhamira ya pamoja ya serikali, wafanyabiashara, taasisi za fedha, washirika wa maendeleo na wadau wote kubadilisha mapendekezo na ushirikiano uliojengwa wakati wa mkutano huo kuwa mipango halisi, uwekezaji na matokeo yanayopimika yatakayoboresha maisha ya wananchi wa kanda ya SADC.


Mabanda ya Benki ya NMB yanaendelea kuwa miongoni mwa vivutio vikuu katika Maonesho ya Nane Nane yanayoendelea katika kanda mbalimbali nchini, huku mawaziri, viongozi wa Serikali na Wananchi wakitembelea kujionea suluhisho za kifedha zinazowezesha kilimo, mifugo, uvuvi na biashara.
Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar, na Naibu Waziri wa Kilimo, David Silinde, wakitembelea banda la Benki ya NMB wakati wa Maonesho ya Nane Nane yanayoendelea jijini Dodoma.
 Naibu Waziri wa Fedha, Laurent Luswetula, akimsikiliza Meneja Mahusiano wa Benki ya NMB Kanda ya Kati kutoka Idara ya Kilimo na Biashara, Miastela Magoma, alipokuwa akipata maelezo kuhusu huduma za benki hiyo alipotembelea banda la NMB kwenye Maonesho ya Nane Nane Kanda ya Mashariki yanayofanyika katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, mkoani Morogoro.

Mwanza: Meneja Mahusiano wa Biashara kwa Serikali wa Benki ya NMB, Humphrey Kaaya (kushoto), akitoa maelezo kwa wakazi wa Mkoa wa Mwanza kuhusu fursa za upatikanaji wa mikopo ya matrekta na suluhisho za kifedha zinazowezesha ununuzi wa zana za kisasa za kilimo, wakati wa Maonesho ya Nane Nane yanayofanyika katika Viwanja vya Nyamhongolo, mkoani Mwanza.

NMB ni mdhamini wa Maonesho ya Nane Nane 2026, ikiwa sehemu ya dhamira yake ya kusogeza huduma za kifedha karibu na wananchi na kuwawezesha wakulima, wafugaji, wavuvi na wajasiriamali kuongeza tija na kukuza uchumi kupitia huduma zinazokidhi mahitaji yao.

Baraza la Michezo la Taifa (BMT) limetangaza fursa 12 zitakazotokana na Tanzania kuwa mwenyeji mwenza wa Mashindano ya Mataifa ya Afrika AFCON 2027 ambazo zitafungua zaidi milango ya maendeleo ya uchumi, ajira, biashara, utalii na uwekezaji nchini.

Akizungumza kuhusu fursa hizo, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma wa BMT, Bw. Aminiel Aligaesha, amesema AFCON 2027 ni tukio la kihistoria litakalofanyika kwa mara ya kwanza Ukanda wa Afrika Mashariki na likiwa linatimiza miaka 70 mwakani tangu kuanzishwa kwake.

Kwa mujibu wa Bw. Aligaesha, fursa ya kwanza ni kuongezeka kwa biashara na shughuli za kiuchumi, ambapo hoteli, nyumba za kulala wageni, migahawa, maduka pamoja na wauzaji wa bidhaa zenye nembo za mashindano watanufaika kutokana na ongezeko la wageni na mashabiki.

Aidha, amesema sekta ya benki na huduma za kifedha itanufaika kupitia ongezeko la miamala ya kifedha, huduma za kubadilisha fedha za kigeni, udhamini wa matukio na utoaji wa bidhaa maalum za kifedha kwa wafanyabiashara watakaohudumia wageni.

Katika upande wa ajira, Bw. Aligaesha amesema vijana watapata nafasi za kazi katika sekta za ukarimu, usafiri, utalii, teknolojia, uandishi wa habari, uzalishaji wa maudhui na huduma nyingine, hali itakayowaongezea uzoefu wa kufanya kazi katika mazingira ya kimataifa.

Pia ametaja sekta ya usafiri kuwa miongoni mwa zitakazonufaika kutokana na kuongezeka kwa mahitaji ya usafiri wa anga, nchi kavu na majini, ikiwemo safari za ndani, huduma za teksi, mabasi, usafiri wa mtandaoni na vifurushi maalum vya safari za AFCON vinavyoweza kujumuisha utalii na malazi.

Kwa mujibu wa Bw. Aligaesha, AFCON 2027 pia itachochea maendeleo ya soka nchini kwa kuhamasisha uwekezaji katika akademi za vijana, ukocha, urefa na ukuzaji wa vipaji, huku sekta ya afya ikitarajiwa kunufaika kupitia utoaji wa huduma kwa wageni na kukuza utalii wa afya kutokana na uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali.

Amesema mashindano hayo yatatoa jukwaa la kutangaza utamaduni wa Tanzania kupitia muziki, vyakula, sanaa, mavazi na lugha ya Kiswahili, sambamba na kuitangaza Tanzania (national branding) kwa mamilioni ya watazamaji duniani kupitia televisheni, mitandao ya kijamii na vyombo vya habari vya kimataifa.

Kuhusu sekta ya utalii, Bw. Aligaesha alisema wageni watakaokuja kushuhudia mashindano hayo watapata nafasi ya kutembelea vivutio mbalimbali ikiwemo Serengeti, Ngorongoro, Mlima Kilimanjaro na Zanzibar, jambo litakaloongeza mapato ya sekta hiyo.

Ameongeza kuwa maandalizi ya AFCON tayari yamechochea maboresho makubwa ya miundombinu ikiwamo ukarabati wa Uwanja wa Benjamin Mkapa, ujenzi wa viwanja vipya Arusha na kule Zanzibar, pamoja na uboreshaji wa barabara, viwanja vya mazoezi na mifumo ya huduma za kidijitali ambayo itaendelea kutumika hata baada ya mashindano hayo kumalizika.

Kwa mujibu wa Bw. Aligaesha, mafanikio ya maandalizi na uendeshaji wa AFCON 2027 yataifanya Tanzania kuwa kitovu cha michezo barani Afrika, huku yakifungua milango ya kuandaa mashindano mengine ya kimataifa, kuvutia wawekezaji na kukuza uchumi wa michezo.

Aidha, amesema mashindano hayo yataimarisha diplomasia ya michezo na ushirikiano wa Afrika Mashariki pamoja na kuimarisha uhusiano wa kikanda katika biashara, utalii, utamaduni na uwekezaji.

Akihitimisha, Bw. Aligaesha amewataka Watanzania kuendelea kufuatilia taarifa za BMT, akieleza kuwa utaratibu rasmi wa namna wananchi na wadau watakavyoweza kushiriki na kunufaika kupitia fursa hizo utatangazwa baadaye mwaka huu.

"Tunatoa wito kwa wananchi, wafanyabiashara na wadau wote kuanza kujiandaa mapema. AFCON 2027 ni mwanzo wa ukurasa mpya wa maendeleo ya michezo na uchumi wa michezo nchini, na muda si mrefu tutatangaza utaratibu wa namna fursa hizi zitakavyopatikana," amesisitiza Bw. Aligaesha.

Na Seif Mangwangi, Michuzi TV Arusha

SERIKALI ya Korea Kusini imesema imefurahishwa na maendeleo ya programu ya kuwezesha wanafunzi wa masomo ya ufundi ya Innovative Energy Education Program (IEEP), kupitia chuo cha ufundi Arusha (ATC), ambayo imekuwa ikifadhiliwa na Serikali yake.

Akizungumza baada ya kutembelea chuo hicho Julai 31 2026, Balozi wa Korea Kusini Nchini Bi. Eunje Ahn amesema Serikali ya Korea Kusini itaendelea ushirikiano na chuo cha ufundi Arusha (ATC), katika fani ya uhandisi wa mitambo na kuhakikisha malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 yanatekelezwa.

Balozi Ahn amesema ameridhishwa na ushirikiano uliokuwepo kati ya Serikali ya Tanzania na Korea Kusini kupitia chuo hicho cha ufundi na kwamba ufadhili ilioutoa miaka saba iliyopita na kutarajiwa kumalizika mwakani umeleta mafanikio makubwa.

Amesema vijana wengi wa kitanzania wamepata ujuzi na ajira kupitia programu hiyo na kwamba amefurahishwa zaidi na ubunifu ambao umekuwa ukifanywa na vijana hao kwa kubuni teknolojia mbalimbali.

" Chuo kikuu cha Hanyang na Seoul ni miongoni mwa vyuo ambavyo vimekuwa vikishirikiana na chuo hiki cha ufundi Arusha kwa walimu na wanafunzi wake kubadilishana ujuzi, na Leo tumefika hapa ATC kuona maendeleo ya programu tuliyokuwa tukiifadhili  kwa miaka saba kuanzia mwaka 2020 na inaelekea ukingoni kumalizika mwakani2027, nimefurahishwa sana na maendeleo mazuri ya programu hii," amesema.

Mkuu wa chuo cha ufundi Arusha (ATC), Profesa Chacha Mussa amesema Serikali ya Korea imekuwa msaada mkubwa chuoni hapo ambapo imekuwa ikifadhili walimu na wanafunzi wanaosomea kozi ya ufundi.

" Ushirikiano wetu na Korea Kusini kupitia vyuo vikuu viwili vya ufundi nchini huko ulipelekea sisi kuanzisha kozi ya Mechatronics and material engineering, ambayo ni ya kwanza nchini na Afrika Mashariki, ni kozi inayotoa waendesha mitambo kwenye viwanda," amesema.

Amesema kozi hiyo ilianzishwa baada ya serikali ya Tanzania chini ya Hatari Dkt John Pombe Magufuli kuamua kujikita katika kuanzisha viwanda na hivyo chuo hicho kuanza mchakato wa kutayarisha vijana watakaoendesha mitambo viwandani.

" Tulianzisha kozi hii baada ya Serikali kuamua kuanzisha viwanda na hivyo watu wa kuendesha mitambo walihitajika sana, vijana wengi wameshapatikana na wako kazini hivi sasa, yote hii ni Kwa ushirikiano na Serikali ya Korea Kusini ambapo walimu na wanafunzi wanapata fursa ya kushirikiana kimasomo," Amesema.

Mkurugenzi wa kampuni ya I- tech Tanzania na Meneja programu ya Innovative Energy Education (IEEP), inayofadhiliwa na Serikali ya Korea Kusini, Dkt Wob Lee amesema Balozi amefurahishwa na mafanikio ya programu hiyo.

Balozi Ahn ametembelea madarasa, maabara na karakana zinanazotumiwa na wanafunzi wa programu hiyo na kuona bunifu mbalimbali zinazoendelea kufanywa, pamoja na karakana kubwa inayoendelea kujengwa ambayo itatumika Kwa kufundishia pamoja na uzalishaji.







 

 Na Mwandishi Wetu 


Na Mwandishi Wetu 

MJUMBE wa Kamati ya Utekelezaji ya Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Taifa, Mariam Abdallah Ibrahim, amefanya ziara ya kikazi katika Wilaya ya Gairo,mkoani Morogoro, kwa lengo la kukagua shughuli za maendeleo zinazotekelezwa na wanawake kupitia umoja huo. 

Katika ziara hiyo, Mariam Ibrahim ambaye pia ni Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Pwani ametembelea  na kukagua vikundi vya wajasiriamali , huku akiwapongeza kwa juhudi zao za kujiongezea kipato na kuchangia maendeleo ya familia pamoja na taifa.

Akizungumza na wananchi na wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) amewashukuru wakazi wa Mkoa wa Morogoro kwa kukichagua Chama Cha Mapinduzi katika Uchaguzi Mkuu kwa kumpatia kura nyingi Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na kuwachagua wabunge na madiwani wa chama hicho.

Pia amewahimiza wanawake kujitokeza kwa wingi kugombea nafasi za uongozi ndani ya CCM, akieleza kuwa ushiriki wao katika nafasi za maamuzi ni muhimu katika kuimarisha maendeleo na kuendelea kutetea maslahi ya wanawake na jamii kwa ujumla.

Mjumbe huyo wa Kamati ya utekelezaji UWT Taifa amefanya ziara hiyo ikiwa ni sehemu ya juhudi za UWT Taifa za kufuatilia utekelezaji wa shughuli za jumuiya hiyo, kuhamasisha maendeleo ya wanawake, na kuimarisha ushiriki wao katika shughuli za kisiasa, kijamii na kiuchumi.











Top News