📍TANESCO yawapa  wazazi na waalimu  elimu ya nishati safi ya kupikia kwa umeme

📍Jiko la Nishati safi ya kupikia latolewa kuendelea kuhimiza matumizi ya kupika kwa umeme 

Katika kuunga mkono jitihada za Serikali za kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia, TANESCO Mkoa wa Kigamboni ilitoa elimu ya matumizi ya umeme kwa ajili ya kupikia katika Shule ya Msingi Malaika iliyopo Kigamboni. 

Elimu hiyo ilitolewa wakati wa siku maalum ya ufunguzi wa shule tarehe 13 Januari, 2026  (Back to School), iliyowakutanisha wazazi na walimu.

Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Afisa Uhusiano na Huduma kwa Wateja wa TANESCO Mkoa wa Kigamboni, Bi. Tumaini Mahwaya, alisema kuwa lengo la kutumia fursa hiyo  ni kuhakikisha wazazi na waalimu wanapata uelewa wa kina kuhusu faida za kutumia nishati ya umeme kupikia akibainisha faida zake kuwa ni nishati salama, gharama nafuu na rafiki kwa mazingira.

“Shirika linakenga kuhakikisha wazazi na walimu wanaelewa kuwa kupikia kwa umeme ni salama, ni nafuu na kunalinda afya pamoja na mazingira. Tukibadili mtazamo wetu leo, tutakuwa tumewekeza kwenye maisha bora ya baadaye,” alisema Tumaini.

Vile vile, ili kuunga mkono utekelezaji wa matumizi ya nishati safi ya umeme katika taasisi za elimu, TANESCO ilikabidhi jiko la umeme aina ya Pressure Cooker lenye ujazo wa kilo 15 kwa uongozi wa shule hiyo ambalo litawarahisishia kupika shuleni hapo. 

Kwa upande wake Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Malaika Bw. Ahmed Abdallah Fataki aliishukuru TANESCO Mkoa wa Kigamboni kwa msaada huo na kuahidi kulitumia kikamilifu, hatua itakayosaidia kuachana na matumizi ya nishati zisizo salama shuleni hapo.

“Jiko hili litatusaidia sana kuboresha huduma za chakula kwa wanafunzi na kutuondolea utegemezi wa nishati zisizo salama. Tunaishukuru TANESCO kwa kutukumbuka na kutuunga mkono katika ajenda ya nishati safi,” alisema Bw. Fataki.

Nao wazazi wa wanafunzi hao walionesha mwitikio mkubwa kwa kutembelea banda la TANESCO kupata elimu kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia na kuahidi kuacha matumizi ya nishati zisizo salama, ili kulinda afya zao na mazingira kwa ujumla.









Na Munir Shemweta, WANMM

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii imeahidi kutoa ushirikiano kwa Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi wakati wote wa kutekeleza majukumu yake.

Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 15 Januari, 2026 na Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Timetheo Mnzava wakati wa kikao cha Kamati ya Kudumu ya Bunge na Wizara ya Ardhi kilichokuwa na lengo la kuifahamu wizara ya ardhi na taasisi zake.

Pamoja na kuifahamu wizara na taasisi zake, Kamati za Kudumu za Bunge zinatakiwa kufahamu baadhi ya sera na sheria kulingana na majukumu ya kila kamati kama ilivyofafanuliwa kwenye nyongeza ya 8 ya Kanuni za Kudumu za Bunge chini ya Kanuni ya 140 ya Kanuni za Bunge inayoelekeza Kamati kupitishwa kwenye majukumu yake ya msingi na Kamati ya Bajeti kufanya maandalizi ya Hoja zitakazojadiliwa na Bunge.

Mwenyekiti huyo wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii ambaye ni Mbunge wa jimbo la Korogwe vijijini amesema, kelele ni nyingi katika masuala ya ardhi lakini wao kama kamati wataendelea kuwa pamoja na wizara kuhakikisha migogoro ya ardhi inatatuliwa na kazi ya kushughulikia changamoto za sekta ya ardhi inakuwa nyepesi.

Kwa upande wake Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo aliwashukuru wajumbe wa kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii kwa michango yao aliyoieleza kuwa ina lengo la kuboresha sekta ya ardhi nchini.

"Sisi wizara tutahakikisha tunapokea ushauri na maoni yenu na kuyafanyia kazi ili tuwe na matokeo chanya katika sekta ya ardhi" amesema mhe Dkt Akwilapo.

Vikao vya Kamati za Kudumu za Bunge ni kwa ajili ya maandalizi ya Mkutano wa 2 wa Bunge la 13 unaotarajiwa kuanza Jumanne, tarehe 27 Januari, 2026.

Kikao hicho kimehudhuriwa na Naibu Waziri wa Wizara hiyo Mhe. Kaspar Mmuya, Katibu Mkuu Mhandisi Anthony Sanga, Naibu Katibu Mkuu Bi Lucy Kabyemera, wajumbe wa Menejimeti pamoja na Wakuu wa taasisi zilizo chini ya Wizara hiyo.
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akizungumza mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii wakati wa kikao cha Kamati na wizara yake kilichokuwa na lengo la kuifahamu wizara ya ardhi na taasisi zake tarehe 15 Januari, 2026Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Kaspar Mmuya akizungumza wakati wa kikao cha Kamati na wizara kilichofanyika jijini Dodoma tarehe 15 Januari, 2026
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii Mhe Timotheo Mnzava akifafanua jambo wakati wa kikao cha kamati yake na Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kilichofanyika jijini Dodoma tarehe 15 Januari 2026
Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii Mhe. Mary Francis Masanja akizungumza wakati wa kikao cha kamati yake na Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kilichofanyika jijini Dodoma tarehe 15 Januari 2026

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akizungumza mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii wakati wa kikao cha Kamati tarehe 15 Januari, 2026.









Washiriki wa kikao cha Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii na Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kilichofanyika jijini Dodoma tarehe 15 Januari 2026

Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Ardhi Maliasili na Utalii ambaye ni mbunge wa viti maalum Khadija Taya maarufu Keysha akizungumza wakati wa kikao cha Kamati tarehe 15 Januari, 2026
Mkurugenzi wa Maendeleo ya Makazi Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Bw. Deogratius Kalimenze akiwasilisha taarifa ya idara yake wakati wa kikao cha Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii na Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kilichofanyika jijini Dodoma tarehe 15 Januari 2026 (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)



●Tanzania yajipanga kuwa kitovu cha uongezaji thamani madini Afrika.

●Yashauri kuhusu ushirikiano wa kikanda na kisekta.


Riyadh, Saudi Arabia

Tanzania imetambua shughuli za uongezaji thamani madini kama nguzo muhimu ya kuleta maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii lengo kubwa ikiwa ni kuondokana na uuzaji na usafirishaji wa madini ghafi kwa nchi zinazozalisha madini mbalimbali Barani Afrika.

Hayo yamebainishwa na Naibu Waziri wa Madini Mhe. Dkt. Steven Kiruswa, wakati akizungumza kwenye Kongamano la Kimataifa la Madini lijukanalo kama Future Minerals Forum 2026 lililowakutanisha mawaziri, viongozi mashuhuri na wadau wa sekta ya madini kutoka zaidi ya nchi 100 ndani na nje ya Bara la Afrika.

Dkt. Kiruswa amesema kuwa, rasilimali madini ni moja ya utajiri mkubwa uliopo Barani Afrika hivyo kuna umuhimu mkubwa wa kuweka mkazo katika shughuli za uongezaji thamani madini ndani ya nchi za Afrika ambapo kama kila nchi itazingatia hilo itakuwa moja ya ufunguo wa kubadilisha utajiri wa madini kuwa kichocheo cha maendeleo endelevu kwa wananchi na taifa kwa ujumla.

Akielezea kuhusu juhudi mbalimbali zinafanywa na Serikali ya Tanzania katika kuendeleza Sekta ya Madini, Dkt. Kiruswa ameeleza kuwa Serikali ya Tanzania inaendelea kuboresha miundombinu ya usafirishaji na mawasiliano ikiwemo ujenzi wa reli ya mwendo kasi, barabara, nishati ya umeme na uongezaji wa bandari ili kuhakiskisha rasilimali zinasafirishwa kwa urahisi kutokea mgodini na kiwandani.

Dkt. Kiruswa amefafanua kuwa, ili kufanikisha hilo ni vyema kila taifa liendeleze viwanda vya uchakataji, uchenjuaji na usafishaji madini akitolea mfano kwa taifa la Tanzania linavyoendeleza juhudi mbalimbali katika mnyororo wa thamani madini ikiwemo kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji, mifumo ya usafirishaji katika ngazi ya kimataifa kupitia Bandari ya Dar es Salaam.

Akisisitiza kuhusu Ushirikiano wa kikanda, Dkt. Kiruswa amesisitiza kuwa, ndani ya Bara la Afrika tunapaswa kushirikiana kwa kuanzisha vituo vya kikanda vya uchenjuaji, uchakataji na usafishaji madini katika nchi zenye miundombinu mizuri ili nchi jirani pia ziweze kuvitumia ikiwa pamoja na kujenga mahusiano ya kisekta kati ya Afrika na Muungano wa kiuchumi na kikanda kati ya nchi za Afrika na nchi za Mashariki ya Kati.

Katika Kongamano hilo la Kimataifa Tanzania imewakilishwa na Naibu Waziri wa Madini, Kaimu Balozi, Ubalozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Riyadh- Saudi Arabia pamoja na wataalam mbalimbali kutoka Wizara ya Madini, Tume ya Madini, Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) na Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST).






Sharjah, 15 Januari 2026

Mke wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Zanzibar Maisha Bora Foundation (ZMBF), Mama Mariam H. Mwinyi, leo tarehe 15 Januari 2026, ametembelea House of Wisdom, maktaba ya kisasa iliyopo Sharjah, inayohifadhi zaidi ya vitabu 300,000 vikiwemo machapisho ya kielimu, fasihi na tafiti mbalimbali.

Maktaba hiyo ni kituo muhimu cha kimataifa katika kuhifadhi na kuwasilisha taarifa za kihistoria za watu mashuhuri kutoka sehemu mbalimbali za dunia. Katika ziara hiyo, Mama Mariam alipata fursa ya kushuhudia urithi wa mashairi ya kale uliowasilishwa kwa mtindo wa kisasa unaochanganya teknolojia, ubunifu na fasihi, hali inayovutia kizazi cha sasa na kijacho kujifunza, kutafsiri na kutumia historia hiyo katika shughuli za maendeleo ya mataifa mbalimbali.

Aidha, Mama Mariam H. Mwinyi alitembelea Soko Asili la Al-Asra lililopo katikati ya mji wa Sharjah, ambako alijionea kazi mbalimbali za mikono zinazofanywa na wasanii wa ndani, wakiwemo vijana wenye ulemavu wa mtindio wa ubongo.

Katika soko hilo, Mama Mariam alipata kuona ubunifu wa vijana hao katika utengenezaji wa misala, pochi za kubebea, vikombe vya kahawa vya aina mbalimbali pamoja na kazi nyengine za mikono zenye ubora, zinazotunza asili na utamaduni wa Kiemarati, na ambazo zimefanikiwa kuuzika sokoni.

Ziara hiyo inaonesha dhamira ya Mama Mariam H. Mwinyi katika kuunga mkono matumizi ya sanaa, fasihi, utamaduni na ubunifu kama nyenzo muhimu ya maendeleo na uwezeshaji wa jamii, hususan makundi maalum.


















Na Mwandishi wetu Iringa


Imeelezwa kuwa zoezi la uandaaji Utekelezaji wa Miongozo ya Ufuatiliaji na Tathmini Serikalini Kunachangia kuongeza kasi ya Ukamilishaji wa Miradi ya Maendeleo kwa kuzingatia mchango wake katika kurahisisha shughuli za utekelezaji wa Miradi mbalimbali na kujiletea maendeleo nchini.

Haya yamezunguzwa na Dkt. James Henry Kilabuko Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu akizungumza kwa niaba ya Dkt. Jim Yonazi Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo wakati wa ufunguzi wa kikao kazi na Wakurugenzi, Maafisa Mipango na Wakuu wa Vitengo vya Ufuatiliaji na Tathmini kutoka Mamlaka za Serikali za Mitaa (MSM), Mkoani Iringa.

Amesema, kikao hiki ni utekelezaji wa maelekezo ya Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya uongozi thabiti wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ili kuimarisha mifumo ya usimamizi wa utendaji, uwajibikaji na kuhakikisha kuwa Afua mbalimbali za Serikali ikiwemo miradi ya maendeleo inatekelezwa kwa ufanisi na kuleta matokeo yaliyokusudiwa kwa wananchi kwa wakati.

Aidha amesema Ofisi ya Waziri Mkuu, ikiwa na jukumu la kikatiba la kuratibu na kusimamia utendaji wa shughuli za Serikali, imeona ni muhimu kukutana ili kujadili kwa kina dhana ya Ufuatiliaji na Tathmini ikiwa na utekelezaji wa miongozo mbalimbali ya Ufuatiliaji na Tathmini ikiwemo Muongozo Jumuishi wa Ufuatiliaji na Tathmini uliotolewa Juni 2024.

"Ofisi ya Waziri Mkuu, iliandaa Muongozo Jumuishi wa Ufuatiliaji na Tathmini, ili kutoa maelekezo elekezi na sanifu yatakayowezesha Serikali kufuatilia, kutathmini na kupima utendaji wa taasisi zote kwa pamoja, kwa kutumia dhana ya "The Whole of Government Approach" Amesema Dkt. Kilabuko

Aidha amewasisitiza Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa, kuhakikisha suala la Ufuatiliaji na Tathmini linafanyika kwa ufanisi na ni wajibu wa Wakurugenzi kuhakikisha kwamba Vitengo vya Ufuatiliaji na Tathmin vilivyoanzishwa mwezi Aprili 2024, vinapewa rasilimali watu na fedha za kutosha, na vinapata ushirikiano kutoka idara zote.

Pia amewataka maafisa Mipango wote nchini Kuhakikisha mipango wanayoiandaa na kuratibu inakwenda sambamba na viashiria vya Ufuatiliaji na Tathmin tangu hatua za awali.

Mwisho amewatakia mafanikio washiriki wote wa kikao kazi hicho na kuwasihi kutumia vizuri muda uliotengwa kwa tija na kujenga mtandao baina yao kwani Serikali tayari imeshaonesha njia na itaendelea kuwaunga mkono katika kutekeleza majukumu ya kila siku.










 Na. Joseph Mahumi na Saidina Msangi, WF, Dodoma


Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amekutana na kufanya mazungumzo na ujumbe kutoka Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu (FIU) ukiongozwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Wataalamu wa Kuzuia Utakasishaji Fedha Haramu ambaye pia ni Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Bi. Sauda Msemo, pamoja na Kamishna wa FIU, Bw. Majaba Magana.

Katika mazungumzo yao yaliyofanyika katika Ofisi ya Waziri wa Fedha, jijini Dodoma, pande hizo zimejadili masuala mbalimbali yanayohusu udhibiti wa utakatishaji fedha haramu, ufadhili wa ugaidi na ufadhili wa silaha za maangamizi, sambamba na mikakati mipya ya kidigitali inayolenga kuboresha mifumo ya ufuatiliaji na udhibiti wa vitendo hivyo.

Waziri wa Fedha amepongeza jitihada za FIU na wadau wengine katika kuhakikisha mifumo ya udhibiti wa fedha haramu inaendelea kuimarika nchini, na kusisitiza umuhimu wa ushirikiano wa taasisi zote zinazohusika katika sekta ya fedha na usalama wa Taifa.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Wataalamu wa Kuzuia Utakatishaji Fedha Haramu ambaye pia ni Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Bi. Sauda Msemo, alisema kuwa Tanzania itakua mwenyeji wa Mkutano wa Kimataifa wa Ubadilishaji wa Taarifa za Udhibiti wa Fedha Haramu Duniani (EGMONT Group meeting) unaotarajiwa kufanyika tarehe 26 hadi 30 Januari 2026, jijini Arusha.

Vilevile, katika kikao hicho, walizungumzia mafanikio ya Tanzania kuondolewa kwenye Orodha ya Nchi zenye Mapungufu ya Kimkakati katika mifumo ya kudhibiti utakasishaji fedha haramu, ufadhili wa ugaidi na ufadhili wa silaha za maangamizi (Grey List) mwezi Juni mwaka jana, hatua ambayo imeongeza imani ya kimataifa kwa mfumo wa fedha wa Tanzania.

Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Naibu Waziri wa Fedha Mhe. Laurent Luswetula (Mb), Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Bw. Elijah Mwandumbya na maafisa wengine waandamizi wa Wizara ya Fedha na FIU.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akizungumza wakati wa kikao kazi cha kupokea taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu - FIU, kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Waziri wa Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.
Naibu Waziri wa Fedha Mhe. Laurent Luswetula (Mb), akizungumza wakati wa kikao kazi cha kupokea taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu, kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Waziri wa Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Bw. Elijah Mwandumbya, akifafanua jambo wakati wa kikao kazi cha kupokea taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu, kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Waziri wa Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.
Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) na Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Wataalamu ya Kuzuia Utakasishaji Fedha Haramu, Bi. Sauda Msemo, akifafanua jambo kuhusu majukumu ya Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu - FIU, katika kikao kazi kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Waziri wa Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.
Kamishna wa Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu - FIU, Bw. Majaba Magana, akieleza kuhusu majukumu yanayotekelezwa na Kitengo cha FIU, katika kikao kazi na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Waziri wa Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.

Waziri wa Fedha wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akiongoza kikao kazi cha kupokea taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu - FIU, kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Waziri wa Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Dodoma)

Top News