Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amesema unapotafakariwa mustakabali wa utoaji huduma za afya nchini, hakuna budi kutoa kipaumbele kwa vijana kama Hayati Benjamini Mkapa alivyoamini, ikiwemo kubuni programu zitakazowaandaa vijana kukabiliana na changamoto za siku zijazo kwa kujiamini.

Makamu wa Rais amesema hayo, wakati alipomwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Mkutano wa Nne wa kuenzi na kuendeleza Urithi wa Hayati Benjamin William Mkapa na Maadhimisho ya Miaka 20 ya Taasisi ya Benjamin Mkapa (BMF), uliyofanyika katika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam. Amesema Vijana ndiyo viongozi wa sekta ya afya wa kesho, watumishi wa afya na watafiti wajao.

Makamu wa Rais amesema Maisha na uongozi wa Hayati Benjamin Mkapa unatoa mafunzo mengi hususani katika usimamizi na uendelezaji wa sekta ya afya nchini kwa kuwa alitambua nafasi ya afya bora katika maendeleo. Ameongeza kwamba, Hayati Benjamin Mkapa katika awamu yake aliweka mkazo katika mapambano dhidi ya UKIMWI, Malaria na magonjwa mengine yanayoambukizwa na yasiyo ya kuambukiza.

Amesema katika uhai wake, Hayati Mkapa aliamini katika kujenga taasisi na alitumia muda wake, nguvu na jitihada zake nyingi kuhakikisha taasisi hizo zinaimarika. Amesema ushahidi upo unaoonesha kuwa taasisi nyingi zilizoasisiwa katika uongozi wake bado zinaendelea kutekeleza majukumu yake ipasavyo.

Makamu wa Rais amesema ni muhimu kiongozi katika sekta ya afya kuelewa uhusiano uliopo kati ya afya na uchumi, siasa, utamaduni, pamoja na muunganiko kati ya mifumo ya afya ya kitaifa na ya kimataifa. Ameipongeza Taasisi ya Benjamin Mkapa kwa kutoa mchango wake kwa sehemu kubwa kuwezesha viongozi katika sekta ya afya.

Halikadhalika, Makamu wa Rais amesema, viongozi wa awamu nyingine akiwemo Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, wameendeleza jitihada za kuimarisha sekta ya afya na kupambana na changamoto zake ikiwemo kusimama kidete kuongoza mapambano dhidi ya UVIKO-19 na magonjwa mengine.

Amesema Serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika kukuza elimu ya sayansi, hususan katika taasisi za elimu ya juu kupitia programu mbalimbali. Makamu wa Rais amepongeza ushirikiano kati ya Taasisi ya Benjamin Mkapa na Wizara ya Afya katika kuanzisha jukwaa la vijana kujadili ajenda ya rasilimali watu katika sekta ya afya.

Makamu wa Rais amewahimiza vijana kutumia kikamilifu fursa zitokanazo na maendeleo ya teknolojia kama akili unde, tiba kwa njia ya mtandao ,uchambuzi wa takwimu na teknolojia mpya zitakazoendelea kubadilisha tasnia ya afya.

Makamu wa Rais ameunga mkono azma ya kuubadilisha Mkutano huo kutoka mkusanyiko wa mara moja kila baada ya miaka miwili, na kuwa jukwaa kuu la Afrika la fikra za kitaalamu, majadiliano ya sera, ubunifu na kubadilishana maarifa kuhusu nguvu kazi ya afya, litakalofanyika mara moja kila mwaka.

Mkutano huo, umehudhuriwa na Mlezi wa Taasisi ya Benjamin Mkapa ambaye ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Viongozi mbalimbali wa Serikali, wadau wa maendeleo wa Kitaifa na Kimataifa, wadau wa sekta ya afya pamoja na wananchi.








Na Mwandishi Wetu
SERIKALI  imesema mafanikio yaliyopatikana kupitia Mradi wa Mifumo ya Maji, Usafi wa Mazingira na Afya (WS4H) yameweka msingi mpya wa kuimarisha huduma endelevu za maji, usafi wa mazingira na afya nchini, huku ikiahidi kuyaingiza katika mipango ya maendeleo ya taifa.

Hayo yalisemwa mjini Morogoro na Mkurugenzi wa Ufuatiliaji na Tathmini wa Wizara ya Maji, Diana Kimario, akimwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mwajuma Waziri, wakati wa hafla ya kuhitimisha mradi huo.

Alisema uzoefu uliopatikana umeonyesha kuwa mafanikio ya sekta ya maji hayaishii katika ujenzi wa miundombinu, bali yanahitaji taasisi imara, mifumo madhubuti ya usimamizi, matumizi ya takwimu sahihi na ushirikiano wa wadau ili kuhakikisha huduma zinakuwa endelevu.

Kimario alisema serikali itaendelea kutumia mafunzo ya mradi huo katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji na Mpango Mkakati wa Sekta ya Afya ili kuongeza ubora wa huduma kwa wananchi.

Alieleza kuwa mradi huo umechangia kuimarisha huduma za maji vijijini kupitia ujenzi wa uwezo wa taasisi, kuboresha mifumo ya takwimu, kuimarisha taaluma na kupanga maendeleo kwa kuzingatia ushahidi, hatua zilizoongeza ufanisi wa utoaji wa huduma.

Aidha, alisema WS4H umeimarisha mipango ya usafi wa mazingira katika halmashauri, ukijumuisha masuala ya mabadiliko ya tabianchi, usawa wa kijinsia na ujumuishi wa makundi mbalimbali, sambamba na kuboresha mifumo ya ufuatiliaji na uwajibikaji katika sekta.

Kimario aliwashukuru Taasisi ya Maendeleo ya Uholanzi (SNV) na Ofisi ya Mambo ya Nje, Jumuiya ya Madola na Maendeleo ya Uingereza (FCDO) kwa kufadhili mradi huo, akizitaka taasisi za serikali na wadau wengine kuendeleza mafanikio yaliyopatikana kwa kuyajumuisha katika mipango na bajeti zao.

Kwa upande wake, Kiongozi wa Sekta ya Maji wa SNV, Olivier Germain, alisema licha ya mradi kufikia mwisho, maarifa, ushirikiano na mifumo iliyoanzishwa itaendelea kuisaidia Tanzania kufikia lengo la kuhakikisha wananchi wote wanapata huduma salama, za uhakika na endelevu za maji, usafi wa mazingira na afya.

Mradi wa WS4H, uliotekelezwa katika mikoa ya Dodoma, Arusha na Simiyu kwa ushirikiano wa Wizara ya Maji, Wizara ya Afya, Ofisi ya Rais–TAMISEMI na RUWASA, umehitimishwa baada ya mkutano uliowakutanisha zaidi ya wajumbe 80 waliotathmini mafanikio yake na kupendekeza hatua za kuyapanua katika maeneo mengine nchini.




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongoza Kikao cha Baraza la Mawaziri kilichofanyika Ikulu Chamwino mkoani Dodoma, tarehe 16 Julai, 2026.


Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Katika kuimarisha juhudi za kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini, waandishi wa habari na maafisa mawasiliano Serikalini wamehimizwa kujenga ushirikiano wa karibu na wadau mbalimbali ili kuongeza ufanisi wa utoaji wa elimu na utekelezaji wa kampeni zinazolenga kufikisha ujumbe kwa wananchi.

Wito huo umetolewa na Mshauri wa Mawasiliano kutoka Kampuni ya Kengo, Niwaeli Gittens-Mbaga, wakati akiwasilisha mada kuhusu nafasi ya vyombo vya habari katika kuendeleza ajenda ya nishati safi ya kupikia kwenye siku ya pili ya warsha ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari pamoja na maafisa mawasiliano kutoka mikoa, wizara na taasisi mbalimbali za Serikali inayofanyika mkoani Morogoro.

Katika mada yake,  Gittens-Mbaga alieleza kuwa mafanikio ya kampeni za nishati safi ya kupikia yanategemea kwa kiwango kikubwa uwezo wa wadau wa mawasiliano kuanzisha na kudumisha mahusiano yenye tija na taasisi, washirika wa maendeleo pamoja na sekta binafsi zinazoweza kuchangia rasilimali na utaalamu.

Aidha, aliwapa washiriki mbinu za kuandaa mapendekezo ya miradi (project proposals) yanayokidhi mahitaji ya wadau mbalimbali, akisisitiza umuhimu wa kuzingatia vipaumbele na maslahi ya kila mdau ili kuongeza nafasi ya kupata ushirikiano na ufadhili wa utekelezaji wa miradi ya kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Baada ya sehemu ya nadharia, washiriki walishiriki mazoezi ya vitendo kwa kugawanywa katika makundi tofauti, ambapo kila kundi liliandaa pendekezo la mradi wa mawasiliano kuhusu nishati safi ya kupikia na kuliwasilisha mbele ya wawezeshaji pamoja na washiriki wengine.

Uwasilishaji huo uliambatana na mjadala na mrejesho wa kitaalamu uliolenga kuboresha ubora wa mapendekezo hayo, huku washiriki wakipata fursa ya kuimarisha uelewa wao kuhusu mbinu bora za kushirikisha wadau na kutumia mawasiliano yenye matokeo katika kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.

Warsha hiyo inaendelea kuwajengea washiriki uwezo wa kitaalamu ili kuwawezesha kuandaa na kusambaza maudhui sahihi yatakayochochea uelewa wa jamii na kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali kufikia malengo ya ajenda hiyo nchini.





Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, ambaye pia ni Msarifu wa Taasisi ya Benjamin William Mkapa Foundation, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema njia bora ya kuuenzi urithi wa Hayati Rais Benjamin William Mkapa ni kuendelea kuwekeza katika uongozi, kuimarisha mifumo ya afya na kuwawezesha vijana kuwa wasanifu wa mustakabali wa Afrika.

Rais Dkt. Mwinyi amesema hayo leo, tarehe 16 Julai 2026, katika Jukwaa la Nne la Kuuenzi Urithi wa Mkapa pamoja na Maadhimisho ya Miaka 20 tangu kuanzishwa kwa Taasisi ya Benjamin William Mkapa Foundation, yaliyofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC), jijini Dar es Salaam.

Amesema Taasisi ya Benjamin William Mkapa Foundation imeendelea kuwa mshirika muhimu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha mifumo ya afya, kuendeleza rasilimali watu wa sekta ya afya na kuboresha huduma za afya ya msingi kwa wananchi.

Katika hafla hiyo, Rais Dkt. Mwinyi alitunukiwa Tuzo Maalumu ya kutambua mchango wake katika maendeleo ya Taasisi ya Benjamin William Mkapa Foundation, iliyokabidhiwa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Emmanuel John Nchimbi. 

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi alimkabidhi Mhe. Dkt. Nchimbi Tuzo ya Juu ya Uongozi katika Mageuzi ya Afya  kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Emmanuel John Nchimbi, Mama Anna Mkapa, Viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mabalozi, Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika, Prof. Mohamed Yakub Janabi, wawakilishi wa Taasisi za kimataifa, Wadau wa maendeleo, wataalamu wa afya na Wageni mbalimbali waalikwa.


















 Vodacom Tanzania PLC imezindua rasmi mashindano ya Gofu ya Vodacom Corporate Masters 2026 kwa kushirikiana na Oakwood Holdings Limited yatayofanyika Lugalo Golf Club, ikiwa ni sehemu ya dhamira yake ya kuimarisha uhusiano wa kibiashara, kukuza ushirikiano na kuleta fursa zenye tija kwa wateja, washirika wa kibiashara na wadau muhimu nchini.

Yakiongozwa na kitengo cha biashara (Vodacom Business), mashindano haya yanatumika kama jukwaa kuu la udhamini wa mchezo wa golf kwa sekta ya biashara, lililobuniwa kuunganisha jumuiya ya wafanyabiashara nchini huku likiimarisha nafasi ya Vodacom kama mshirika wa kuaminika katika teknolojia na huduma za mawasiliano kwa taasisi na mashirika yanayoendelea kukua katika mazingira ya uchumi wa kidijitali.

Mashindano haya yanayotarajiwa kuanza tarehe 1 Agosti 2026, yatawakutanisha wakuu wa makampuni, wafanyabiashara, wataalamu kutoka sekta mbalimbali, wapenzi wa mchezo wa golf pamoja na wateja wa Vodacom ambao watashiriki katika mfululizo wa mashindano hayo pamoja na matukio ya kujenga mitandao ya kibiashara yatakayofanyika kwenye uwanja wa Lugalo Golf Club.

Mpango huu unaakisi dhamira ya Vodacom Business ya kujenga mahusiano yenye thamani yanayovuka mipaka ya biashara za kawaida kwa kutoa jukwaa la ushirikiano, kubadilishana maarifa, ubunifu na kukuza maendeleo endelevu.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkuu wa Idara ya Masoko na Uwezeshaji wa Vodacom Tanzania Plc, Joseph Sayi alisema mashindano hayo yanadhihirisha dhamira ya Vodacom ya kuimarisha uhusiano wake na jumuiya ya wafanyabiashara nchini Tanzania na ndio maana wameamua kudhamini kwa mwaka wa tatu mfululizo.

"Vodacom tunaamini kuwa ukuaji endelevu wa biashara unajengwa kupitia mahusiano imara na yenye maana. Mashindano ya golf ya Vodacom Corporate Masters 2026 ni zaidi ya mashindano ya michezo, hili ni jukwaa linalowakutanisha viongozi wa biashara, wabunifu na watoa maamuzi ili kujenga uhusiano, kubadilishana mawazo na kusaka fursa mpya zitakazochangia ajenda ya Tanzania ya mageuzi ya kidijitali. Kupitia mpango huu tunaendelea kuziwezesha biashara kwa kutoa suluhisho za teknolojia zenye uhakika huku tukiwapa wateja na wadau wetu uzoefu wa kipekee," alisema Sayi.

Katika kipindi chote cha mashindano hayo, Vodacom Business itaonesha suluhisho zake bunifu za kidijitali zinazojumuisha huduma za mawasiliano, usalama wa kidijitali pamoja na teknolojia za biashara zinazosaidia taasisi kuongeza ufanisi wa shughuli zake, kuharakisha ukuaji na kuendelea kuwa na ushindani katika dunia inayozidi kutegemea teknolojia. Washiriki pia watapata fursa ya kukutana na viongozi wa Vodacom na kupata uelewa wa suluhisho mbalimbali zinazokidhi mahitaji yanayobadilika ya biashara.

Mwenyekiti wa Corporate Masters, Ken Kariuki alielezea mashindano hayo kuwa ni jukwaa la kipekee la ushirikishwaji wa makampuni linalowezesha kuongeza muonekano wa chapa, kujenga mitandao ya kibiashara, kuzalisha fursa za biashara na kuimarisha ushiriki wa wateja.

Tukio hilo la siku moja litashirikisha timu 10 za makampuni zitakazoshindania kombe la Vodacom Corporate Masters 2026, sambamba na eneo maalum la makampuni litaklokuwa na burudani, maonesho mbalimbali, maonesho ya vitu vya kale (vintage) pamoja na eneo maalum la watoto, hivyo kuweka mazingira rafiki kwa familia, kwa washiriki na wageni watakaohudhuria.

Mashindano ya golf ya Vodacom Corporate Masters yanaendelea kudhihirisha dhamira ya Vodacom Tanzania ya kujenga ushirikiano wa kuaminika na kuunga mkono mipango inayozalisha thamani ya kudumu kwa wateja, biashara na jamii. Kwa kuunganisha michezo, biashara na ubunifu, Vodacom inaendelea kuimarisha nafasi yake kama mshirika wa kuaminika katika safari ya Tanzania kuelekea uchumi wa kidijitali.
Mkuu wa Idara ya Masoko na Uwezeshaji wa Vodacom Tanzania Plc, Joseph Sayi (katikati) akizungumza wakati wa kutangaza udhamini wa Mashindano ya Golf ya Vodacom Corporate Masters 2026, yaliyoandaliwa kwa ushirikiano na  Lugalo Golf Club kwa lengo la kuunganisha jumuiya ya wafanyabiashara nchini Tanzania, kuimarisha mahusiano ya kibiashara, kukuza ushirikiano na kuleta fursa zenye tija kwa wateja, washirika wa kibiashara na wadau muhimu nchini. Mashindano hayo yatakayofanyika tarehe 1 Agosti 2026 yanaendelea kuimarisha nafasi ya Vodacom kama mshirika wa kuaminika katika teknolojia na huduma za mawasiliano kwa taasisi na mashirika yanayoendelea kukua katika mazingira ya uchumi wa kidijitali. Uzinduzi huo umefanyika tarehe 16 Julai 2026 jijini Dar es Salaam na kushuhudiwa na Katibu wa Corporate Masters, Maryanne Mugo (kushoto) pamoja na Mwenyekiti wa Kamati ya Corporate Masters, Ken Mbaya (kulia).







MAMLAKA ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira mjini Moshi (MUWSA) imeendelea na jitihada zake za kuhakikisha upatikanaji wa maji katika kata ya Marangu Mashariki wilayani Moshi mkoani Kilimanjaro unakuwa ni wa uhakika ambapo wameendelea kuboresha miundombinu kwa kununua mabomba mapya ya kulaza umbali wa kilomita 13.

Akizungumza mara baada ya kuwasili kwa mabomba hayo, Mkuu wa Idara ya Ufundi, Mhandisi Innocent Lugodisha alisema kuwa, mradi huo unatekelezwa kwa awamu mbili ambapo mamlaka tayari imeshakamilisha awamu ya kwanza ya mradi.

Mhandisi Lugodisha alisema kuwa, mradi huo unatarajiwa kugharimu shilingi 1,470,121,709 ambapo awamu ya kwanza 234,355,900 na awamu ya pili utatumia 1,235,765,808.

"Mradi huu ukikamilika utasaidia upatikanaji wa maji katika vijiji vya Samanga, Rauya na Ashira kuwa wa uhakika ambapo utaongeza uzalishaji maji kutoka mita za ujazo 402 hadi 4320 kwa siku na mahitaji kwa vijiji hivi ni mita za ujazo 1164" alisema Mhandisi Lugodisha.

Alisema kuwa, awamu ya kwanza ulihusisha ujenzi wa chanzo cha Lyasongoro na Kyerio, ujenzi wa uzio katika chanzo, ujenzi wa break pressure na ulazaji wa bomba zenye urefu wa kilomita 2.4.

Aliongeza kuwa, katika awamu ya pili kazi zitakazoenda kufanyika ni uchimbaji wa mtaro na ulazaji wa bomba lenye kipenyo cha inchi 8 na 6 lenye urefu wa kilomita 13.

Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Vunjo, Enock Koola alisema kuwa, mradi huo utakapokamilika utasaidia kuondoa tatizo la maji kabisa katika vijiji vya Rauya, Samanga na Ashira ambavyo vilikuwa vikipata maji chini ya asilimia 50.

"Wakati wa ziara ya Waziri Mkuu mkoani Kilimanjaro niliwasilisha changamoto ya upatikanaji maji katika jimbo letu hususani kata hii ya Marangu mashariki na Waziri Mkuu alimwagiza Waziri wa maji kuhakikisha upatikanani maji kwa wananchi unatatuliwa na aliahidi kulitatua ndani ya muda mfupi na matokeo yameanza kuonekana kupitia mradi huo" alisema Koola.








Na Mwandishi wetu, Mirerani 

MWENGE wa uhuru umekagua na kutembelea mradi wa viti 120 na meza 120 za wanafunzi wa shule ya sekondari Tanzanite ya Kata ya Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara.

Mkuu wa shule ya sekondari Tanzanite, Jude Samwel Mziray ameeleza hayo wakati akisoma taarifa ya mradi huo kwa kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru mwaka 2026 Wazo Mwang'onda.

Mwalimu Mziray amesema shule ya sekondari Tanzanite ilipokea viti na meza hizo Mei 28, mwaka 2026.

Amesema shule hiyo ilipokea viti 120 na meza 120 kwa ajili ya maandalizi ya kuwapokea wanafunzi wa kidato cha kwanza 2028 watakaohitimu darasa la sita na la saba kwa wakati mmoja 2027.

"Mradi huu umezingatia kigezo namba 53 cha namna Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro ilivyoandaa miundombinu ya kupokea wanafunzi wa kidato cha kwanza mwaka 2028," amesema.

Amesema mradi huo umetengewa kiasi cha shilingi 10,800,000.00 kutoka katika mapato ya Halmashauri ya Wilaya na fedha iliyotumika ni shilingi 10,560,000.00 

"Ndugu kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru kitaifa mradi huu umetekelezwa kwa kutumia mfumo wa kielektroniki wa manunuzi ya Taifa (NaST) na fundi aliyetengeneza viti 120 na meza 120 ni Ibrahim Elias Mmary.

Amesema mafanikio ya mradi huo wa viti na meza ni kupunguza idadi ya wanafunzi wasiokuwa na viti na meza watakaoingia kidato cha kwanza 2028 na vyumba vitatu kuanza kutumika.

"Tunaishukuru Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuboresha mazingira ya kujisomea na kujifunzia katika shule hii," amesema mwalimu Mziray.

Hata hivyo, kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru kitaifa mwaka 2026 amepongeza mradi huo ambao utakuwa na manufaa makubwa kwa wanafunzi hao.

Mwang'onda amewaasa wanafunzi wa shule hiyo watakaotumika madawati na meza hizo kuzitunza ili waweze kutumia kwa muda mrefu.



Sekta ya mifugo nchini inatarajiwa kuingia katika hatua mpya ya utoaji wa huduma kufuatia kuanzishwa kwa zana za kidijitali za Mfumo wa Ulezi wa Kitaaluma kwa Maduka ya Dawa za Mifugo (Agrovet Mentoring Framework–AMF) na Mfumo wa Ulezi wa Kitaaluma kwa Watoa Huduma za Afya ya Mifugo (Animal Health Mentoring Framework–AHMF), ambazo zinalenga kuongeza ubora, uwajibikaji na weledi katika sekta hiyo.

Akizungumza katika kikao cha wadau kilichowakutanisha taasisi mbalimbali za sekta ya mifugo Jijini Dodoma, Msajili wa Baraza la Madaktari wa Mifugo Tanzania, Dkt. Amani Kilemile, alisema mfumo wa sasa unaotumia nyaraka za karatasi katika kufuatilia na kusimamia wataalamu wa mifugo pamoja na wahudumu wa maduka ya dawa za mifugo umekuwa ukikabiliwa na changamoto mbalimbali, zikiwemo ugumu wa kufuatilia utendaji wa wataalamu, kuhifadhi kumbukumbu sahihi na kusimamia uzingatiaji wa viwango vya taaluma.

Alisema matumizi ya zana hizo za kidijitali yatamwezesha mlezi wa kitaaluma kufanya tathmini ya umahiri wa mtaalamu kwa wakati halisi, kurekodi maendeleo yake na kutoa mrejesho wenye muundo unaoeleweka, hatua itakayoongeza uwajibikaji na kuboresha ubora wa huduma zinazotolewa kwa wafugaji.

Dkt. Kilemile aliongeza kuwa tofauti na mfumo wa awali wa karatasi, zana hizo zitamwezesha mlezi kushuhudia utendaji wa kila siku wa mtaalamu, kubaini mapungufu ya uwezo, kutoa mafunzo ya vitendo na kufuatilia maendeleo yake kwa karibu ili kuhakikisha viwango vya kitaaluma vinaendelea kuzingatiwa.

Alisema mifumo hiyo pia itasaidia kusimamia maeneo muhimu ikiwemo uzingatiaji wa sheria na kanuni za taaluma, utoaji bora wa huduma kwa wateja, usambazaji unaowajibika wa dawa za mifugo, usimamizi wa stoo za dawa na bidhaa za mifugo pamoja na kuimarisha maadili ya taaluma.

Zana hizo zimetengenezwa na Brooke East Africa, shirika la ustawi wa wanyama lenye makao yake nchini Kenya, na zinatekelezwa nchini Tanzania na INADES-Formation Tanzania kwa kushirikiana na Arusha Society for Protection of Animals (ASPA), kwa lengo la kujenga uwezo wa wataalamu wa afya ya mifugo na wahudumu wa maduka ya dawa za mifugo.

Kwa upande wake, Wizara inayosimamia sekta ya mifugo ilieleza kuwa mfumo huo wa kidijitali utarahisisha ukusanyaji na uchambuzi wa taarifa, kuongeza ufanisi wa usimamizi na kuwezesha maamuzi yanayotegemea ushahidi, tofauti na mfumo wa karatasi ambao umekuwa ukisababisha ucheleweshaji wa taarifa na changamoto za ufuatiliaji.

Mkurugenzi Mtendaji wa INADES-Formation Tanzania, Bi. Jacqueline Nicodemus, pamoja na wawakilishi wa ASPA na Brooke East Africa, walisisitiza dhamira yao ya kuendelea kushirikiana na Serikali kuhakikisha mifumo hiyo inatekelezwa kwa ufanisi ili kuleta mageuzi katika sekta ya mifugo.

Wadau walieleza matumaini kuwa matumizi ya mifumo ya AMF na AHMF yataongeza uwezo wa wataalamu wa mifugo, kuboresha afya na ustawi wa wanyama, kuongeza uzalishaji wa mifugo, kuhamasisha matumizi sahihi ya dawa za mifugo na kujenga imani zaidi kwa wafugaji kupitia huduma zenye ubora, weledi na uwajibikaji.






Top News