Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, akisalimiana na Kiongozi Mkuu wa Kanisa Katoliki Duniani, Baba Mtakatifu Leo XIV, mara baada ya Ibada ya Hija iliyofanyika katika Uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro – Vatican, leo tarehe 01 April 2026


Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) imemkaribisha rasmi Mkurugenzi Mtendaji mpya, CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi, katika ofisi za Makao Makuu ya Bodi hiyo jijini Dodoma, Aprili 1, 2026, ikiwa ni hatua ya kuanza rasmi kwa utekelezaji wa majukumu yake.

Akizungumza mara baada ya kuwasili ofisini hapo, CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi alisisitiza umuhimu wa ushirikiano kwa wafanyakazi, akibainisha kuwa mafanikio ya Taasisi yoyote yanategemea mshikamano, uwajibikaji na ufanisi wa kila mfanyakazi.

“Ni muhimu kila mmoja wetu akatimiza wajibu wake kwa ufanisi na kwa kuzingatia maadili ya kazi, ili kuendelea kujenga taswira nzuri ya Taasisi,” alisema CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi.

Aidha, alitumia fursa hiyo kusikiliza na kupokea kero pamoja na maoni mbalimbali kutoka kwa wafanyakazi, huku akiahidi kuyafanyia kazi kwa lengo la kuboresha mazingira ya utendaji kazi na kuongeza ufanisi ndani ya Taasisi.

Sambamba na hilo, CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi alikutana na Mhasibu Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, CPA Leonard Mkude, ofisini kwake jijini Dodoma, kwa lengo la kufahamiana na kuendeleza uhusiano wa kikazi uliopo kati ya ofisi hiyo na NBAA.

Katika mazungumzo yao, CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi alisisitiza dhamira ya kushirikiana kwa karibu na serikali pamoja na wadau wa Taaluma ya Uhasibu ili kuhakikisha Taaluma hiyo inaendelea kukua na kufikia viwango vya kimataifa.

“Tutashirikiana na Serikali na wadau mbalimbali wa Taaluma ya Uhasibu kuhakikisha kuwa Taaluma yetu inaendelea kuwa na viwango vya kimataifa, pamoja na kuimarisha uwazi na mawasiliano kwa wananchi,” alisema CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili katika ofisi za Makao Nakuu ya Bodi hiyo yaliyopo jijini Dodoma.
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi akizungumza jambo alipokuwa akitembelea ofisi za Bodi hiyo jijini Dodoma.
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi akizungumza na baadhi ya wafanyakazi wa NBAA alipowasili katika ofisi za Makao Makuu ya Bodi hiyo jijini Dodoma.
Baadhi ya wafanyakazi wa NBAA wakimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji wa NBAA, CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi alipokuwa akizungumza na wafanyakazi wa Bodi alipowasili katika ofisi za Makao Makuu ya Bodi hiyo jijini Dodoma.
Mhasibu Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, CPA Leonard Mkude akizungumza na Mkurugenzi Mtendaji mpya wa NBAA, CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi alipofika kujitambulisha katika ofisi yake jijini Dodoma akisindikizwa na baadhi ya viongozi wa NBAA.
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

CHUO Kikuu Mzumbe, Ndaki ya Dar es Salaam katika kituo chake cha Tegeta, kimetoa elimu ya uelewa kwa wanawake 200 kuhusu usimamizi wa mirathi, ikiwa ni jitihada za kupunguza migogoro ya kifamilia inayotokana na masuala ya urithi.

Akizungumza Aprili 1, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa semina hiyo, Rasi wa Chuo hicho, Prof. Cyricus Binamungu, amesema mafunzo hayo ni sehemu ya mpango endelevu wa kuwakutanisha wanajamii ili kuwajengea uelewa mpana juu ya masuala ya mirathi.

Amesema usimamizi wa mirathi ni suala nyeti, huku mali nyingi zikibaki katika akaunti za mahakama zikisubiri kuchukuliwa na warithi kutokana na migogoro isiyoisha miongoni mwa familia.

“Unakuta mali nyingi zipo mahakamani zinasubiri warithi, lakini migogoro inapochelewesha taratibu, mali hizo haziwafikii walengwa kwa wakati,” amesema Prof. Binamungu.

Ameongeza kuwa wanaamini elimu hiyo itasaidia kupunguza kwa kiasi kikubwa migogoro hiyo na kuwezesha familia kusimamia vyema urithi wao.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Tegeta, Bered Ntabaliba, amekipongeza chuo hicho kwa kuwafikishia wananchi elimu hiyo muhimu, akieleza kuwa itawasaidia wanawake kujisimamia na kufuatilia masuala ya mirathi kwa ufanisi zaidi.

Amesema eneo la Tegeta limekuwa likikumbwa na migogoro mingi ya mirathi, hivyo semina hiyo itachangia kupunguza changamoto hiyo kwa kuwapa wananchi uelewa wa sheria na taratibu husika.

“Hili ni somo muhimu sana kwetu, litasaidia wananchi kuelewa namna ya kurithi mali na kuepuka migogoro ya kifamilia,” amesema Ntabaliba.

Baadhi ya washiriki wa semina hiyo wameishukuru Mzumbe kwa kuwapatia mafunzo hayo, huku wakitoa wito kwa taasisi nyingine kuendelea kutoa elimu kama hiyo ili kupunguza migogoro inayojitokeza katika jamii, hususan ndani ya familia.















Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Katika kukabiliana na changamoto kama mabadiliko ya tabianchi na upotevu wa bio-anuai, watafiti nchini wamehimizwa kuhakikisha tafiti zao zinatoa suluhisho la moja kwa moja kwa jamii badala ya kubaki kwenye maandiko ya kitaaluma pekee.

Wito huo umetolewa leo Aprili 1, 2025 na wadau mbalimbali wa sekta ya utafiti wakati wa mkutano wa kuadhimisha miaka 50 ya jarida la Tanzania Journal of Science (TJS) uliofanyika katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).

Imeelezwa kuwa tafiti za kisayansi zina mchango mkubwa katika kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050, hivyo kuna umuhimu wa kuhakikisha matokeo yake yanawafikia wananchi pamoja na watendaji kwa utekelezaji.

Akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Daniel Mushi, amesema watafiti wana wajibu wa kuhakikisha tafiti wanazozifanya zinakuwa chachu ya maendeleo ya taifa.

Amebainisha kuwa Tanzania inalenga kufikia uchumi wa dola za Kimarekani trilioni moja ifikapo mwaka 2050, sambamba na kuongeza kipato cha mtu mmoja mmoja kufikia wastani wa dola 7,000 kwa mwaka.

Ameongeza kuwa mafanikio hayo hayawezi kupatikana bila kuongeza tija katika sekta zote za uzalishaji kupitia tafiti zenye manufaa kwa jamii.

Katika hatua nyingine, ametoa tahadhari kwa watafiti na wahariri wa majarida ya kitaaluma kuhusu matumizi yasiyo sahihi ya teknolojia ya Akili Unde (AI), akisema inaweza kutumika vibaya kuzalisha taarifa zisizo za kweli na kuhatarisha uaminifu wa tafiti.

“Watafiti wasiokuwa makini wanaweza kutumia AI kutengeneza taarifa za uongo, jambo ambalo linaweza kuharibu sifa na uaminifu wa majarida ya kisayansi nchini,” amesema.

Kwa upande wake, Mratibu wa mkutano huo, Profesa Andrew Macrice kutoka UDSM, amesema maadhimisho hayo hayalengi tu kusherehekea mafanikio ya miaka 50 iliyopita, bali pia kuweka mikakati madhubuti kwa miaka ijayo.

Ametaja baadhi ya changamoto zinazohitaji tafiti makini kuwa ni pamoja na upotevu wa ardhi, mabadiliko ya tabianchi, uhaba wa chakula na kupungua kwa bio-anuai.

Nae Makamu Mkuu wa UDSM, Profesa William Anangisye, amesema sayansi inapaswa kushirikiana na jamii na kusaidia katika utungaji wa sera zinazogusa maisha ya wananchi moja kwa moja.

Amesema kuwa jarida la TJS limekuwa nyenzo muhimu katika kuwajenga watafiti chipukizi na kutoa jukwaa la kubadilishana mawazo ya kitaaluma.

Pamoja na hayo ametoa wito kwa watafiti vijana kutumia fursa ya maadhimisho hayo kama chachu ya kukuza taaluma zao, akisisitiza kuwa mustakabali wa sayansi nchini unategemea nidhamu, uadilifu na ubunifu.

Jarida la TJS, ambalo ni miongoni mwa majarida 27 yanayomilikiwa na UDSM, limeendelea kupata mafanikio kwa kuingia katika mifumo ya kimataifa ya uchapishaji, hatua inayoongeza ushindani na mwonekano wa tafiti za Tanzania duniani.


















Top News