Na Munir Shemweta, Dodoma

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii imekutana leo tarehe 12 Agosti 2026 Bungeni jijini Dodoma kupokea na kujadili taarifa kuhusu utendaji wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya, ikiwa ni sehemu ya jukumu la Bunge la kusimamia na kufuatilia utekelezaji wa majukumu ya Serikali katika sekta ya ardhi.

Katika kikao hicho, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeieleza Kamati hatua mbalimbali zilizochukuliwa katika kuboresha utendaji wa Mabaraza hayo, ambayo yako chini ya Wizara hiyo.

Miongoni mwa hatua zilizobainishwa ni kuongezeka kwa idadi ya Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya, kupungua kwa mashauri na malalamiko, kuimarishwa kwa matumizi ya mifumo ya kidijiti pamoja na kuboreshwa kwa mfumo wa uendeshaji wa shughuli za madalali.

Pamoja na mafanikio hayo, Kamati imeelezwa kuwa bado zipo changamoto kadhaa zinazoathiri utendaji wa Mabaraza hayo na kwamba Wizara inaendelea kuzifanyia kazi ili kuongeza ufanisi na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Kaspar Mmuya, amewaeleza wajumbe wa Kamati kuwa, Serikali inaendelea kushughulikia changamoto zinazoyakabili Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya, akieleza kuwa kutatuliwa kwa changamoto hizo kutasaidia kuyafanya Mabaraza kuwa bora zaidi na yenye manufaa makubwa kwa wananchi.

 

Awali, wajumbe wa Kamati wameitaka Wizara kuweka mkazo zaidi katika matumizi ya usuluhishi wakati wa kushughulikia migogoro ya ardhi badala ya kila shauri kulenga kupata mshindi na mshindwa.

Wamesema, usuluhishi unaweza kusaidia kupunguza migogoro, kuharakisha utatuzi wa mashauri na kujenga mahusiano mazuri miongoni mwa wananchi.

Wajumbe hao wameeleza kuwa, pamoja na mafanikio yanayoonekana katika utendaji wa Mabaraza, bado ipo haja ya Wizara kuchukua hatua za haraka kukabiliana na changamoto zilizopo ili Mabaraza hayo yaweze kufanya kazi kwa ufanisi zaidi na kuendelea kujenga imani ya wananchi.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Timotheo Mzava, amesisitiza umuhimu wa Wizara kuongeza idadi ya wenyeviti wa Mabaraza, kupanua upatikanaji wa Mabaraza katika wilaya mbalimbali pamoja na kukamilisha mfumo wa kidijiti ili kuongeza ufanisi na kupunguza malalamiko kutoka kwa wananchi.

“Sisi kama Kamati tunaona umuhimu wa kuwa na Mabaraza kila Wilaya pamoja na kukamilika kwa mfumo wa kidijiti, kwa kuwa mtakapoboresha, kelele kuhusu Mabaraza zitapungua,” amesema Mhe. Mzava.


Kikao hicho kilichoongozwa na Mhe. Mzava pia kimehudhuriwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhandisi Anthony Sanga, Naibu Katibu Mkuu Bi. Lucy Kabyemera, pamoja na viongozi na watendaji wengine wa Wizara.Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Kaspar Mmuya akizungumza mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utali wakati Kamati hiyo ilipokutana na wizara ya Ardhi tarehe 12 Agosti 2026 Bungeni jijini Dodoma kupokea na kujadili taarifa kuhusu utendaji wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya.
Mbunge wa jimbo la Newala Mjini mkoani Mtwara Mhe. Rashid Mtima akichangia mada wakati Kamati ya Kudumu ya Bunge Ardhi na Maliasili ilipokutana na Wizara ya Ardhi Bungeni jijini Dodoma kupokea na kujadili taarifa kuhusu utendaji wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya tarehe 12 Agosti 2026.Mbunge wa jimbo la Hanang’ mkoani Manyara Mhe. Asia Halamga akizungumza wakati Kamati ya Kudumu ya Bunge Ardhi na Maliasili ilipokutana na Wizara ya Ardhi Bungeni jijini Dodoma kupokea na kujadili taarifa kuhusu utendaji wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya tarehe 12 Agosti 2026.Mhe. Taska Mbogo, Mbunge wa viti maalum akizungumza wakati Kamati ya Kudumu ya Bunge Ardhi na Maliasili ilipokutana na Wizara ya Ardhi Bungeni jijini Dodoma kupokea na kujadili taarifa kuhusu utendaji wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya tarehe 12 Agosti 2026.

Washiri wa Kamati ya Kudumu ya Bunge Ardhi na Maliasili na Utalii wakiwa katika kikao cha kupokea na kujadili taarifa kuhusu utendaji wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya tarehe 12 Agosti 2026 jijini Dodoma.
Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhandisi Anthony Sanga akizungumza mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utali wakati Kamati hiyo ilipokutana na wizara ya Ardhi tarehe 12 Agosti 2026 Bungeni jijini Dodoma kupokea na kujadili taarifa kuhusu utendaji wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya. (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)

Na George Maziku, Geita 

HOSPITALI ya Gakala iliyopo kijiji cha Masumbwe, kata ya Bukandwe, wilaya ya Mbogwe inategemea kupokea jopo la madaktari bingwa watakaotoa huduma mbalimbali kuanzia tarehe 17 Agosti, mwaka huu mpaka tarehe 21.

Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi Mkuu wa hospitali hiyo Bunga Dadu Gakala wakati alipozungumza na jopo la waandishi wa vyombo mbalimbali vya habari ofisini kwake.

Alisema kuwa lengo la kuendesha kambi hiyo ni kuwapunguzia wananchi wa wilaya ya Mbogwe na wilaya zingine jirani, gharama za kufuata huduma za matibabu zinazotolewa na madaktari bingwa.

“Hospitali ya Gakala inawatangazia wakazi wa Masumbwe kuwa kutakuwa na madaktari bingwa kuanzia Jumatatu tarehe 17 mpaka 21, mwezi huu. Tutapokea madaktari bingwa 5 wa magonjwa ya kina mama, daktari bingwa wa watoto, daktari bingwa wa upasuaji, daktarin bingwa wa mifupa na daktari bingwa wa magonjwa ya ndani kama vile sukari, presha na magonjwa mengine yote ya ndani.

“Kwahiyo tunawakaribisha sana wananchi wote wa  Masumbwe na maeneo mengine mbalimbali ya wilaya ya Mbogwe na hata wilaya za jirani, waje wapate huduma za mabingwa wa tiba”, alisema Gakala.

Amezitaja huduma zitakazotolewa na madaktari hao kwa kina mama kuwa ni afya ya uzazi, ushauri na vipimo kabla ya ujauzito, matatizo ya kutopata mtoto (Ugumba), uangalizi kipindi cha ujauzito, Ultrasound kwa wajawazito na wasio wajawazito na kutokwa uchafu au damu isiyo kawaida sehemu za siri.

“Pia madaktari hao watatoa matibabu ya uvimbe katika nyonga au tumbo, uchunguzi wa saratani ya mlango wa kizazi na matatizo yatokanayo na hedhi na ukomo wa hedhi”, alifafanua Gakala.

Mkurugenzi huyo amesema kuwa imekuwa kawaida kwa hospitali yake kupokea madaktari bingwa kwa lengo la kuwapatia wananchi wa Masumbwe fursa ya kupata huduma za matibabu karibu na makazi yao badala ya kusafiri mbali kutafuta huduma hizo.







Tunapoelekea kuadhimisha Siku ya Tiba Asili ya Mwafrika tarehe 31 Agosti 2026, Afrika inakabiliwa na swali moja kubwa: Je, tutaendelea kutumia urithi wa tiba asilia kama ulivyo, au tutautafiti, kuuthibitisha, kuuboresha na kuugeuza kuwa sehemu ya suluhisho la afya na uchumi wa kizazi kijacho?

Na TRAMEPRO

Kuna wakati ambapo mgonjwa hakuhitaji kufika hospitalini ili kupata huduma ya afya.

Alikwenda kwa mzee wa kijiji anayejua mmea fulani. Alitafuta mzizi uliokuwa ukitumika kwa vizazi. Alitumia majani, magome, matunda au vyakula vilivyojulikana katika jamii yake.

Maarifa hayo hayakuandikwa katika vitabu vingi.

Hayakuwa kwenye hifadhidata za kisasa.

Lakini yalikuwepo.

Yalihifadhiwa katika kumbukumbu za wazee, waganga wa jadi na jamii zilizojifunza kuishi kwa karibu na mazingira yao.

Hiyo ndiyo sehemu ya historia ya Tiba Asili ya Mwafrika.

Lakini sasa dunia imebadilika.

Maabara zimechukua nafasi kubwa katika utafiti. Teknolojia imebadilisha namna tunavyohifadhi na kuchanganua taarifa. Sayansi imeweka viwango vipya vya kuthibitisha usalama na ufanisi wa dawa.

Na mbele ya mabadiliko hayo, Afrika inapaswa kujiuliza:

Je, tutauacha urithi huu kuwa kumbukumbu ya vizazi vilivyopita, au tutaufanya kuwa msingi wa maarifa, utafiti, ubunifu, ajira na huduma bora za afya kwa vizazi vijavyo?

Hili ndilo tafakari linalokuja wakati Afrika ikijiandaa kuadhimisha Siku ya Tiba Asili ya Mwafrika tarehe 31 Agosti 2026.

Kauli mbiu ya mwaka huu inasema:

“Tafakari kuhusu Juhudi za Utafiti na Maendeleo katika Tiba Asilia kuelekea Kufikia Huduma Bora za Afya kwa Wote katika Kanda ya Afrika.”

Kwa Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira Tanzania (TRAMEPRO), maadhimisho haya hayapaswi kuwa siku ya hotuba na sherehe pekee.

Yanapaswa kuwa nafasi ya kuangalia tulikotoka, tulipo sasa na tunakotaka kwenda.

Tiba Asili ni urithi, lakini urithi pekee hautoshi

Kwa karne nyingi, jamii za Afrika zimekuwa zikitumia rasilimali za mazingira yao katika kukabiliana na changamoto mbalimbali za afya.

Maarifa hayo yamekuwa sehemu ya utamaduni na maisha ya jamii.

Lakini kuna tatizo kubwa linaloendelea kukua.

Maarifa mengi yako hatarini kupotea.

Wataalamu na wazee wanaobeba maarifa hayo wanazeeka. Baadhi wanafariki bila kuyaandika au kuyaacha katika mfumo ambao unaweza kutumiwa na kizazi kijacho.

Wakati huohuo, mazingira yanayozalisha mimea hiyo nayo yako katika hatari.

Misitu inapungua. Uharibifu wa mazingira unaongezeka. Mabadiliko ya tabianchi yanaendelea kubadilisha mifumo ya ikolojia, huku uvunaji holela ukitishia baadhi ya rasilimali za mimea tiba.

Kwa maana hiyo, tunapozungumzia kulinda Tiba Asili, hatuzungumzii dawa pekee.

Tunazungumzia pia kulinda maarifa, mazingira na bioanuwai.

Afrika inatumia Tiba Asili — lakini tunajua kiasi gani?

Matumizi ya Tiba Asili katika Kanda ya Afrika ni makubwa, na WHO imekuwa ikisisitiza umuhimu wake katika maisha ya jamii nyingi.

Hata hivyo, ukubwa wa matumizi hayo unapaswa kutusukuma kwenye swali jingine muhimu:

Tuna takwimu za kutosha kuhusu hali halisi ya Tiba Asili Tanzania leo?

Tunapaswa kujua idadi ya wataalamu waliopo, vituo vya huduma, aina za tiba zinazotumika, bidhaa zinazopatikana, mimea muhimu, tafiti zinazofanyika na mchango wa sekta hii katika ajira na uchumi.

Tunahitaji pia kujua ni watu wangapi wanatumia huduma hizi na kwa sababu zipi.

Kwa sababu sekta haiwezi kupangwa vizuri bila takwimu.

Na bila mipango madhubuti, ni vigumu kujua wapi pa kuelekeza uwekezaji.

Dunia nayo imeanza kuangalia upande huu

Kinachovutia zaidi ni kwamba Tiba Asili sasa si mjadala wa Afrika pekee.

Dunia imeanza kuiangalia kwa mtazamo mpana zaidi.

Mwaka 2025, Mkutano wa 78 wa Afya Duniani uliidhinisha WHO Global Traditional Medicine Strategy 2025–2034, ukiweka mkazo kwenye ushahidi, usalama, ubora, udhibiti na ujumuishaji unaofaa wa Tiba Asili katika mifumo ya afya.

Hii ni ishara kwamba mjadala umebadilika.

Tiba Asili haipaswi tena kuonekana kama jambo lililobaki nyuma katika historia.

Inaweza kuwa sehemu ya mjadala wa afya ya baadaye — ikiwa itaendelezwa kwa utafiti, ushahidi na viwango.

Hapo ndipo Afrika inapaswa kuwa makini.

Kwa sababu kama rasilimali na maarifa haya yana thamani, Afrika haipaswi kuwa mtumiaji wa mwisho wa thamani inayotokana na urithi wake yenyewe.

Afrika inapaswa kuwa mtafiti.

Afrika iwe mvumbuzi.

Afrika iwe mzalishaji.

Afrika iwe mmiliki wa thamani.

Tatizo si ukosefu wa maarifa

Tanzania na Afrika hazikosi maarifa.

Tuna wataalamu wa Tiba Asili.

Tuna mimea yenye thamani.

Tuna vyuo vikuu.

Tuna watafiti.

Tuna wataalamu wa famasia, kemia, botania, mazingira na teknolojia.

Tuna taasisi zinazoweza kushirikiana.

Changamoto kubwa ni namna ya kuunganisha nguvu hizi zote.

Utafiti unatakiwa kufika maabara.

Maabara ziunganishwe na majaribio yanayofaa.

Matokeo ya utafiti yaende kwenye mifumo ya usajili na udhibiti.

Bidhaa salama ziende kwenye uzalishaji.

Uzalishaji uende kwenye masoko.

Na baada ya bidhaa kutumika, kuwe na mfumo wa kufuatilia usalama na madhara yake.

Hapo ndipo tunapoanza kujenga Tiba Asili yenye ushahidi.

Usalama si adui wa Tiba Asili

Katika safari hii, kuna jambo moja ambalo halipaswi kupuuzwa: usalama wa mgonjwa.

Tiba yoyote inayotumika kwa binadamu inahitaji kuangaliwa kwa umakini.

Je, ina ubora unaotakiwa?

Je, kipimo chake kinajulikana?

Je, inaweza kuwa na madhara?

Je, inaweza kuingiliana na dawa nyingine?

Je, imehifadhiwa vizuri?

Na endapo mtumiaji atapata madhara, je, kuna mfumo wa kuyatambua na kuyafuatilia?

Maswali haya hayakusudii kuua Tiba Asili.

Kinyume chake.

Yanalenga kuijenga.

Tiba Asili yenye ubora, usalama, ufanisi na mfumo mzuri wa ufuatiliaji inaweza kuwa na nafasi kubwa zaidi katika mfumo wa afya.

Bila mazingira, hakuna Tiba Asili

Fikiria mmea unaotumika kwa vizazi vingi lakini unapotafutwa miaka kadhaa ijayo haupo tena.

Hapo tunapoteza vitu viwili kwa wakati mmoja: mmea na maarifa yanayohusiana nao.

Ndiyo maana uhifadhi wa mazingira unapaswa kwenda sambamba na maendeleo ya Tiba Asili.

Misitu, ardhi, vyanzo vya maji na bioanuwai ni sehemu ya msingi ya mustakabali wa tiba zinazotokana na mazingira.

Tunahitaji mashamba ya mimea tiba.

Tunahitaji kilimo endelevu.

Tunahitaji kupunguza uvunaji holela.

Tunahitaji tafiti kuhusu uzalishaji na uhifadhi wa mimea tiba.

Na zaidi ya yote, tunahitaji kuhakikisha kwamba kizazi kijacho hakibaki na vitabu vinavyoeleza mimea ambayo tayari imetoweka.

Kutoka mmea hadi bidhaa: Fursa iliyopo kwenye uchumi

Kuna fursa nyingine kubwa ambayo mara nyingi haizungumzwi vya kutosha: uchumi wa Tiba Asili.

Afrika haipaswi kuendelea kuuza malighafi kwa bei ndogo, halafu kununua bidhaa iliyotengenezwa kutokana na malighafi hiyo kwa bei kubwa.

Mnyororo wa thamani unapaswa kujengwa hapa hapa Afrika.

Mmea → Shamba → Utafiti → Maabara → Uzalishaji → Bidhaa → Soko.

Mfumo huo unaweza kuunganisha afya na kilimo, mazingira na viwanda, utafiti na biashara, pamoja na ajira kwa vijana.

Kwa hiyo, Tiba Asili inaweza kuwa zaidi ya suala la tiba.

Inaweza kuwa ajenda ya uchumi.

Wataalamu wanapaswa kuikumbatia sayansi

Kwa wataalamu wa Tiba Asili, huu si wakati wa kuogopa utafiti.

Ni wakati wa kuutumia.

Tusiogope ushahidi.

Tusiogope viwango.

Tusiogope teknolojia.

Tusiogope ushirikiano.

Badala yake, vitu hivi vitumike kuinua taaluma na kuongeza imani ya jamii.

Mtaalamu wa Tiba Asili wa kizazi kipya anapaswa kuwa zaidi ya mtoa huduma.

Anapaswa kuwa mtunza maarifa, mshirika wa utafiti, mtetezi wa mazingira na sehemu ya uzalishaji wa suluhisho salama za afya.

Hii ndiyo njia ya kuunganisha urithi wa wazee na uwezo wa vijana.

Tanzania inahitaji ajenda mpya

Kuelekea 31 Agosti 2026, TRAMEPRO inaona umuhimu wa kuanzisha mjadala mpana wa kitaifa kuhusu Ajenda Mpya ya Tiba Asili Tanzania.

Ajenda hiyo inapaswa kuangalia utafiti wa mimea tiba na dawa asilia, uhifadhi wa maarifa ya jadi, usalama na ufanisi, udhibiti wa bidhaa, uwekezaji, uzalishaji na matumizi ya teknolojia.

Pia kunahitajika hifadhi ya kitaifa ya maarifa ya Tiba Asili inayolinda haki za jamii na kuhakikisha kwamba wenye maarifa wanatambuliwa na kunufaika.

Teknolojia inaweza kuwa sehemu muhimu ya safari hii.

Hifadhidata za mimea, mifumo ya kidijitali ya usajili na ufuatiliaji, pamoja na teknolojia mpya ikiwemo Artificial Intelligence (AI), zinaweza kusaidia kuhifadhi maarifa na kuongeza uwezo wa kufanya utafiti.

Serikali, watafiti na sekta binafsi wanapaswa kukaa meza moja

Hakuna taasisi moja inayoweza kujenga mustakabali wa Tiba Asili peke yake.

Serikali inahitajika katika sera na udhibiti.

Vyuo vikuu vinahitajika katika elimu na utafiti.

Wataalamu wa Tiba Asili wanahitajika katika maarifa na uzoefu wa jamii.

Wanasayansi wanahitajika katika uchambuzi na uthibitishaji.

Sekta binafsi inahitajika katika uwekezaji, uzalishaji na masoko.

Wadau wa mazingira wanahitajika katika uhifadhi wa rasilimali.

Na vijana wanahitajika katika ubunifu na teknolojia.

Hii ndiyo sababu ushirikiano kati ya taaluma mbalimbali si chaguo tena.

Ni hitaji.

Vijana ndio daraja la kesho

Mustakabali wa Tiba Asili hauwezi kubaki mikononi mwa kizazi cha wazee pekee.

Kuna vijana wanaosoma botania.

Wengine famasia.

Wengine kemia.

Wengine teknolojia ya habari.

Wengine kilimo.

Wengine biashara na ujasiriamali.

Kila mmoja anaweza kuwa sehemu ya kujenga Tiba Asili ya kizazi kipya.

Tunachohitaji ni mazingira yatakayowawezesha kuunganisha maarifa ya jadi na taaluma za kisasa.

Hapo ndipo urithi unageuka kuwa ubunifu.

Tarehe 31 Agosti isiwe mwisho wa mjadala

Maadhimisho ya mwaka huu yanapaswa kuacha maswali yenye majibu na hatua zinazoonekana.

Baada ya tarehe 31 Agosti 2026, tutakuwa tumefanya nini?

Je, kutakuwa na utafiti mpya?

Je, tutakuwa tumeanza kuhifadhi maarifa zaidi?

Je, kutakuwa na uwekezaji mkubwa zaidi katika mimea tiba?

Je, bidhaa salama zaidi zitakuwa zimefika sokoni?

Je, vijana wengi zaidi watakuwa wameingia kwenye sekta?

Je, tutakuwa na takwimu bora kuhusu Tiba Asili Tanzania?

Na je, ushirikiano kati ya Tiba Asili na Tiba ya Kisasa utakuwa umeimarika?

Hapo ndipo tutakapopima mafanikio ya maadhimisho.

Kwa sababu maadhimisho bora si yale yenye hotuba nyingi, bali yale yanayoacha hatua nyuma yake.

Tunatafakari leo, tunajenga kesho

Tiba Asili ya Afrika ina historia ndefu.

Lakini historia pekee haitoshi.

Tunapaswa kuichukua historia hiyo na kuipeleka mbele kwa kutumia utafiti, sayansi, teknolojia, ubunifu na viwango.

Tunahitaji kuhifadhi maarifa bila kuyafungia kwenye kumbukumbu.

Tunahitaji kuyatafiti bila kupoteza thamani yake ya kijamii.

Tunahitaji kuyaendeleza bila kuhatarisha usalama wa wananchi.

Na tunahitaji kuongeza thamani bila kuharibu mazingira.

Huo ndio mwelekeo unaoweza kuifanya Tiba Asili kuwa sehemu ya suluhisho la changamoto za afya, mazingira na uchumi barani Afrika.

Kwa hiyo, kuelekea Siku ya Tiba Asili ya Mwafrika, 31 Agosti 2026, TRAMEPRO inatoa wito kwa Serikali, wataalamu, watafiti, vyuo vikuu, taasisi za afya, sekta binafsi, mashirika ya kiraia, wadau wa mazingira na jamii kwa ujumla:

TUIJENGE TIBA ASILI YENYE USHAHIDI.

TUIJENGE TIBA ASILI SALAMA.

TUIJENGE TIBA ASILI YENYE VIWANGO.

TUIJENGE TIBA ASILI INAYOLINDA MAZINGIRA.

TUIJENGE TIBA ASILI INAYOTOA AJIRA NA THAMANI KIUCHUMI.

NA TUIJENGE TIBA ASILI INAYOCHANGIA HUDUMA BORA ZA AFYA KWA WOTE.

Kwa sababu mwisho wa yote, Tiba Asili siyo tu tulikotoka.

Ni sehemu ya tunakokwenda.

🌿 TIBA ASILI YENYE USHAHIDI — AFYA BORA KWA WOTE — MAZINGIRA ENDELEVU KWA VIZAZI VIJAVYO.

Heri ya Maadhimisho ya Siku ya Tiba Asili ya Mwafrika — 31 Agosti 2026.

BONIVENTURA F. MWALONGO
Katibu Mkuu
Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira Tanzania (TRAMEPRO)


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akimkabidhi Meneja wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF), Zanzibar, Bi. Mariam Saleh Tuzo ya shukran kutokana na mchango wa Mfuko huo kuwa miongoni mwa Taasisi zilizofanikisha kufanyika kwa Kongamano hilo ambalo ni sehemu ya Tamasha la 10 la Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar usiku wa kuamkia leo Agosti 12, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akiwa katika picha ya pamoja na Wawakilishi wa Taasisi zilizopatiwa tuzo

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (Kushoto) na mkewe Mama Mariam Mwinyi (mwenye raba nyekundu), wakitembelea mabanda ya Maonesho baada ya kuzindua Tamasha la Kizimkazi Agosti 12, 2026



Meneja wa PSSSF Zanzibar, Bi. Mariam Saleh, akiwa na Tuzo ya shukrani baada ya kukabidhiwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan baada ya kukabidhiwa



Zanzibar, Agosti 12, 2026

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameutunuku Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) tuzo ya kutambua mchango wake katika kuwezesha kufanyika kwa Mdahalo wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia, uliofanyika Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar, usiku wa kuamkia leo, Agosti 12, 2026.

Tuzo hiyo imekabidhiwa kwa Meneja wa PSSSF Zanzibar, Bi. Mariam Saleh, kwa niaba ya Mfuko, ikiwa ni sehemu ya utambuzi kwa taasisi na wadau walioshiriki katika kuwezesha mdahalo huo, uliofuatiwa na Maonesho ya Picha za Tamasha la Kizimkazi.

Mdahalo huo umefanyika sambamba na Tamasha la 10 la Kizimkazi (Kizimkazi Festival 2026), linalofanyika Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar, ambapo tamasha hilo limeanza rasmi leo kwa matembezi pamoja na uzinduzi uliofanywa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi.

Ushiriki wa PSSSF katika mdahalo huo unaakisi dhamira ya Mfuko ya kushirikiana na Serikali, taasisi na wadau mbalimbali katika kuunga mkono mijadala yenye umuhimu kwa jamii, mazingira na maendeleo endelevu.

Aidha, PSSSF inawakaribisha wanachama na wananchi kutembelea banda la Mfuko katika Maonesho ya Tamasha la Kizimkazi yanayoanza leo, Agosti 12, 2026, kwa ajili ya kupata elimu na huduma mbalimbali zinazotolewa na Mfuko, amesema Afisa Uhusiano Mkuu wa PSSSF, Bi. Fatma Elhady.


Mwisho
Na Mwandishi wa OTR

 Ofisi ya Msajili wa Hazina (OTR) Jumanne, Agosti 11, 2026, ilifanya mazungumzo na kampuni ya Fitch Ratings Ltd ikiwa ni sehemu ya mapitio ya pili ya mwaka 2026 ya tathmini ya Fitch Ratings, katika mchakato unaohusisha taasisi mbalimbali za Serikali.

Mazungumzo hayo yanalenga kuwapa wachambuzi wa Fitch Ratings fursa ya kupata taarifa za kina kuhusu mwenendo wa uchumi wa Tanzania, utekelezaji wa sera za kibajeti na fedha, pamoja na mikakati ya Serikali katika usimamizi wa deni la Taifa.

Kwa upande wa OTR, mjadala ulijikita katika utendaji wa taasisi za umma, mageuzi yanayoendelea, vihatarishi vya kifedha, pamoja na mtiririko wa fedha kati ya Serikali na taasisi za Umma.

Mapema mwaka huu, Fitch Ratings iliendelea kuipa Tanzania daraja ‘B+’ kwa hadhi ya ulipaji wa madeni ya muda mrefu ya fedha za kigeni, ikitaja mwelekeo imara wa ukuaji wa uchumi na uwezo wa Serikali kukabiliana na changamoto za kifedha baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.

Fitch inakadiria kuwa uchumi wa Tanzania utakua kwa asilimia 6 kwa mwaka 2026, kiwango ambacho ni kikubwa zaidi ya wastani wa asilimia 4.5 kwa nchi zenye daraja la ‘B’.

Katika muktadha huo, Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, aliyeongoza timu ya OTR, aliieleza timu ya Fitch kuhusu mageuzi yanayolenga kuboresha utendaji na ufanisi wa taasisi za umma, kuimarisha utawala bora na uwajibikaji, pamoja na kupunguza utegemezi wa taasisi hizo kwa Serikali.

Alisema ajenda ya mageuzi ya OTR katika kipindi cha miaka miwili iliyopita imeweka mkazo zaidi katika uongozi, usimamizi wa utendaji na uwajibikaji, ikiwemo kuboresha ubora wa Bodi na timu za menejimenti na kuimarisha tathmini za Bodi ili kubaini mapungufu ya ujuzi.

Bw. Mchechu alisema matokeo ya mageuzi hayo yanaendelea kuonekana katika mchango wa kifedha wa taasisi za umma kwa Serikali.

Katika mwaka wa fedha ulioishia Juni 30, 2026, taasisi zilizo chini ya Msajili wa Hazina zilichangia takribani Sh1.881 trilioni kwa Serikali kupitia gawio na michango mingine, ikilinganishwa na Sh1.028 trilioni katika mwaka wa fedha uliotangulia.

“Tunachokiona ni utayari wa taasisi kuanza kuchangia, au kuongeza mchango wao kwa Serikali,” alisema Bw. Mchechu.

Aliongeza kuwa taasisi zinazoendelea kuhitaji msaada wa Serikali zinatarajiwa kuonesha namna zinavyopunguza utegemezi huo.

Alisema hatua za urekebishaji na uwekezaji wa mtaji zilizochukuliwa katika taasisi kama Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) zimesaidia kupunguza majukumu hayo na kuimarisha hali ya kifedha ya taasisi hizo.

Timu ya Fitch pia iliomba taarifa kuhusu mipango ya kuorodhesha baadhi ya taasisi za umma katika soko la mitaji.

Bw. Mchechu alisema Benki ya Biashara Tanzania (TCB) ni miongoni mwa taasisi zinazotayarishwa kuorodheshwa katika soko la mitaji kupitia uuzaji wa hisa kwa umma kwa mara ya kwanza (IPO), huku Shirika la Taifa la Bima (NIC) likifanyiwa tathmini kwa ajili ya uwezekano wa kuorodheshwa katika soko hilo.

Lengo la muda mrefu ni kurekebisha, kuimarisha na kuorodhesha katika soko la mitaji taasisi kadhaa za umma zinazofaa kabla ya mwaka 2030.

Bw. Mchechu alisema pia OTR imezipa taasisi 58 za umma uhuru zaidi wa kiutendaji, unaoziruhusu kutekeleza majukumu yao kwa mujibu wa mamlaka walizopewa bila kuingiliwa katika utekelezaji wa majukumu yao.

Alisema mageuzi hayo yameimarisha pia uwezo wa ndani wa OTR, hususan katika uchambuzi wa biashara, na hivyo kuiwezesha Ofisi kufanya uchambuzi wa kina zaidi wa bajeti, uwekezaji na mipango ya kimkakati ya taasisi za umma.

Msajili wa Hazina alisema ushirikiano kati ya OTR na Wizara zinazosimamia sekta mbalimbali umeimarika, huku uhusiano huo ukielekezwa zaidi katika kuhakikisha taasisi za umma zinatekeleza vipaumbele vya Serikali.

“Si suala tena la kusema ‘unapaswa kufanya hili na si lile’, bali ‘unafanyaje ili taasisi hii itekeleze kile ambacho Mhe. Rais anataka?’” alisema Bw. Mchechu.

Ujumbe wa Fitch uliongozwa na Bw. José Mantero, Mkurugenzi Mshirika na mchambuzi mkuu anayeshughulikia Tanzania, akifuatana na Bi. Gaimin Nonyane, Mkurugenzi wa Kitengo cha Sovereign and Supranational Group cha Fitch Ratings, na Bw. Gerard Arabian, Makamu wa Rais na Mshauri wa Masuala ya Serikali ‘Sovereign Advisor’ katika Kitengo cha Public Sector Group Corporate Banking.

Bw. Mantero alisema Fitch ililenga kupata uelewa mpana zaidi kuhusu ajenda ya mageuzi ya OTR katika mashirika ya umma, hususan juhudi za kuboresha utendaji wa taasisi na kusimamia madeni na mtiririko wa fedha kati ya Serikali na taasisi za umma.

Alisema mapitio hayo pia yanatathmini athari za maendeleo yanayoendelea katika Mashariki ya Kati kwa Tanzania, ikiwemo athari zinazoweza kujitokeza katika fedha za Serikali, urari wa malipo na mfumuko wa bei kutokana na mabadiliko ya bei za mafuta na mbolea.

Akizungumzia hali chanya ya kifedha ya Serikali inayotokana na uhusiano wake wa kifedha na taasisi za umma, Bw. Mantero alisema: “Hii ni habari njema sana kwa hali ya fedha za Serikali.”

Kwa upande wake, Bi. Nonyane alionekana kuvutiwa na kuongezeka kwa mchango wa mashirika ya umma, akibainisha kuwa mchango huo wa hivi karibuni ulikuwa sawa na takribani asilimia 0.8 ya Pato la Taifa.

Alitaka pia kufahamu namna hali hiyo ilivyobadilika kutoka kipindi ambacho baadhi ya mashirika ya umma nchini yalikuwa yakikabiliwa na changamoto za kifedha.

Mwelekeo huo unaongeza matumaini kwamba mageuzi yanayoendelea yataimarisha zaidi utendaji na uendelevu wa kifedha wa taasisi za umma, kuongeza mchango wao katika uchumi na mapato ya Serikali, pamoja na kuunga mkono juhudi pana za Tanzania za kudumisha uimara wa kifedha na kuboresha hadhi yake ya mikopo.

Taarifa zilizotolewa katika mazungumzo ya OTR na Fitch Ratings yatachangia katika tathmini pana ya kampuni hiyo kuhusu uwezo wa Tanzania wa kutimiza majukumu yake ya kifedha, ikiwa ni sehemu ya mapitio ya pili ya mwaka 2026 ya tathmini ya hadhi ya Tanzania ya ulipaji wa madeni ya Serikali.









Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imetakiwa kuangalia namna ya kupeleka huduma za uchunguzi na matibabu ya magonjwa ya moyo nchini Comoro kutokana na huduma hizo kutopatikana nchini humo.

Rai hiyo imetolewa leo na Balozi wa Tanzania nchini Comoro Mhe. Dkt. Salim Hamad alipotembelea Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI Dkt. Peter Kisenge kuona namna ambavyo huduma zinazotolewa na JKCI zinaweza kuwakomboa wananchi wa Comoro.

Dkt. Hamad alisema baada ya JKCI kuweka kambi maalumu ya matibabu ya moyo katika kisiwa cha Anjouan kilichopo nchini Comoro uongozi wa kisiwa hicho umeitaka JKCI kuingia mkataba nao wa kuendelea kufanya kambi za matibabu jambo ambalo linaonesha umahiri wa huduma zinazotolewa na wataalamu wa JKCI.

“Nilifurahi nilipokutana na uongozi wa kisiwa cha Anjouan na kuniomba niwajulishe kuwa wanataka tuingie nao mkataba wa kufanya kambi za matibabu, hii ni hatua kubwa kwa nchi yetu katika kutoa huduma bingwa za matibabu ya moyo”, alisema Dkt. Hamad.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema uhitaji wa huduma za matibabu ya moyo nchini Comoro ni mkubwa kutokana na mwitikio uliokuwepo wakati wa kambi ya matibabu iliyofanyika mwezi Oktoba mwaka jana katika kisiwa cha Anjouan.

“Tunaandaa mkakati wa kuitangaza JKCI nchini Comoro ili tuweze kuwasaidia wananchi wa Comoro kufahamu zaidi huduma tunazozitoa na kuwapunguzia adha ya kuzifuata huduma hizi mbali na nchi ya Comoro”, alisema Dkt. Kisenge.






Na Victor Masangu, Kibaha

Jumuiya ya umoja wa wanawake (UWT) Wilaya ya Kibaha mjini kwa kushirikiana na wadau wengine wa maendeleo wakiwemo Azania bank wameamua kuungana kwa pamoja na kuitoa darasa la mafunzo kwa wajasiriamali kutoka kata zote 14 kwa lengo la kuweza kuwapa ujuzi wa kutengeneza bidhaa mbali mbali ambazo zitawasaidia kujikwamua kiuchumi.

Akizungumza katika ziara maalumu ya kikazi yenye lengo la kuweza kutoa mafunzo hayo Mwenyekiti wa UWT Wilaya ya Kibaha mjini Elina Mgonja amebainisha kwamba ameamua kutoa darasa hilo ikiwa ni ahadi yake ambayo aliitoa wakati wa zira ya kushukuru wanawake kwa kuweza kuipigia CCM kura za kishindo katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.

Mwenyekiti Mgonja amesema kwamba ametembelea wanawake hao na kutoa fursa za mafunzo ya ujarisiamali kwa kuwafundisha jinsi ya kutengeneza bidhaa za aina tofauti zikiwemo utengenezaji wa sabubi kwa ajili ya kufulia nguo , sabuni ya kuogea, na namna ya kutengeneza batiki pamoja na utengenezaji wa bidhaa nyingine.

"Nikiwa kama Mwenyekiti wa UWT Wilaya ya Kibaha mjini nimeamua kutimiza ahadi yangu ya kuwapa mafunzo ya ujariamali bure wanawake kutoka kata zote 14 zilizopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha na mafunzo haya pia nimeshirikiana na wenzetu wa Azania bank ambao na wao wameweza kutoa elimu ya jinsi ya kutunza fedha na kujikwamua kiuchumi,"amebainisha Mwenyekiti Mgonja.

Kwa upande wake Afisa Mahusiano wa Azania Bank Happiness Lema amebainisha kwamba lengo lao kubwa la kushirikiana bega kwa bega na Jumuiya ya ya wanawake wa UWT Wilaya ya Kibaha mjini kwa lengo la kuwasaidia kuwapa elimu ya kujikwamua kichumi ikiwemo pamoja na suala zima la utunzaji wa fedha.

"Sisi kama Azania bank tumeoana kuna umuhimu mkubwa wa kuweza kushirikiana na Jumujiya ya wanawake wa UWT Wila ya Kibaha mjini na tumeamua kutembea nao katika ziara yakeo yenye lengo la kutoa darasa maaalumu kwa ajili ya kuwafundisha jinsi ya kutengeneza bidhaa na sisi kama benki tumewafundisha namna bora ya kujikomboa kiuchumi pamoja na jinsi ya kutumia fursa za mikopo yenye liba nafuu,"amenainisha Happiness.

Ziara ya Mwenyekiti wa UWT Wilaya ya Kibaha mjini ya kutoa mafunzo kwa wanawake wajasiriamali kwa sasa inaendelea kufanyika ambapo hadi sasa imeshapita katika kata tisa ambazo ni Msangani, Mkuza, Maili moja, Tumbi, Viziwaziwa, Kibaha, Kongowe, Misugususgu pamoja na Kata ya Visiga.






Kizimkazi, Unguja 📍

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umefanikiwa kusambaza takribani mitungi laki saba ya gesi ya kupikia (LPG) nchini kote, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa kasi wa Mkakati wa Kitaifa wa Nishati Safi ya Kupikia.

Hayo yameelezwa na Mkurugenzi wa Nishati Jadidifu na Teknolojia za Nishati Jadidifu kutoka REA, Mhandisi, Advera Mwijage, wakati akizungumza kwenye mdaharo maalum uliofanyika katika Tamasha la Kizimkazi mkoani wa Kusini Unguja, Zanzibar; Mhandisi Advera alimwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Hassan Saidy.

Mhandisi Advera alieleza kuwa mafanikio hayo yametokana na uwezeshaji mkubwa kutoka kwa Serikali ya Awamu ya Sita, pamoja na uwepo wa vyanzo vingi vya nishati nchini. Alibainisha kuwa REA ilitumia majukwaa ya Waheshimiwa Wabunge kusambaza mitungi hiyo ili kuwafikia wananchi wa ngazi ya chini na kutoa elimu ya matumizi ya nishati hiyo.

"Miradi hii ikiwemo ya gesi ya kupikia (LPG) na majiko banifu inatolewa kwa njia ya ruzuku. Bila ruzuku kwa wananchi wa vijijini, mabadiliko ya kuelekea nishati safi yatachukua muda mrefu sana," alisema Mhandisi Advera.

Kuhusu utunzaji wa mazingira, Mhandisi Advera alisema REA imeanzisha mradi wa kusambaza majiko banifu ili kupunguza kasi ya uharibifu wa misitu. Inakadiriwa kuwa takribani hekta 470,000 za misitu hukatwa kila mwaka nchini kwa ajili ya kuni na mkaa.

Ili kukabiliana na changamoto hiyo, REA imeshirikiana na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) kufungua viwanda vya kuzalisha mkaa mbadala maeneo ya vijijini, tofauti na hapo awali ambapo viwanda hivyo vilikuwa vimejificha mijini. Hatua hiyo imefanya mkaa mbadala kupatikana kwa gharama nafuu vijijini.

Katika hatua nyingine, REA kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), imefanikiwa kuunganisha jumla ya wateja 1,001 wa majumbani na taasisi kwenye mkuza wa mabomba ya Gesi Asilia katika mikoa ya Lindi na Pwani.

Mhandisi Advera alitoa wito kwa wananchi ambao bado hawajafikiwa na miradi hiyo kuendelea kuwa wavumilivu, kwani utekelezaji unaenda kwa awamu kulingana na ukomo wa bajeti ya serikali. Lengo kuu la serikali ni kuhakikisha zaidi ya asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia.

Mdaharo huo ulihudhuriwa na viongozi waandamizi wa sekta ya nishati, akiwemo Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, Naibu Waziri Mhe. Salome Makamba, na Katibu Mkuu (Umeme na Nishati Jadidifu) Mhandisi Felchesmi Mramba.

Viongozi wengine waliohudhuria na kushiriki ni pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, huku mdaharo huo ukianzishwa na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Mstaafu, Mhe. Doto Biteko, Mbuge wa Jimbo la Bukombe.









 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Tamasha la Kizimkazi limeendelea kuwa jukwaa muhimu la kutangaza utamaduni, utalii, biashara na fursa za uwekezaji zilizopo Zanzibar, sambamba na kuchochea maendeleo ya wananchi.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 12 Agosti 2026, alipokuwa akizindua rasmi Tamasha la Kizimkazi 2026 lenye kaulimbiu “KIZIMKAZI Kumenoga!” katika Mkoa wa Kusini Unguja.

Amepongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa maono ya kuasisi Tamasha hilo, ambalo limekuwa likichangia kuhifadhi mila na utamaduni, kukuza utalii na kufungua fursa za kiuchumi kwa wananchi.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amesisitiza umuhimu wa kutumia Tamasha hilo kutangaza fursa za uwekezaji katika utalii, uvuvi, mwani na Uchumi wa Buluu, huku Serikali ikiendelea kuimarisha mazingira ya uwekezaji na miundombinu ya uzalishaji.

Amesema Tamasha la Kizimkazi linaunga mkono dhamira ya Serikali ya kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea Zanzibar kutoka 800,000 hadi milioni 1.5, kupitia matukio maalum ya utalii na utangazaji wa vivutio, utamaduni, vyakula na ukarimu wa Wazanzibari.

Rais Dkt. Mwinyi amewapongeza waandaaji, wadhamini, taasisi za Serikali, Sekta Binafsi, wajasiriamali, wasanii, wanamichezo na wananchi kwa kufanikisha Tamasha la Kizimkazi 2026, akihimiza kuendelea kulitumia kama jukwaa la kufungua fursa mpya za maendeleo.

Tamasha hilo linaendelea hadi tarehe 14 Agosti 2026, ambapo kilele chake kitafanyika katika Uwanja wa Mwehe, Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja.




















Top News