▪️︎ Azindua Mfumo wa Kitaifa wa Taarifa za Uwezeshaji Kiuchumi (NEMIS)

▪️︎ Ataka wigo wa miradi kwa Watanzania kupanuliwa

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, ametoa wito wa kuhakikisha Watanzania wanashiriki kikamilifu katika uchumi wa nchi yao, akisisitiza kuwa uwezeshaji wa wananchi ni msingi wa kuongeza ajira, kukuza sekta binafsi, kuongeza mapato na kupunguza umaskini.

Dkt. Mwigulu ameyasema hayo leo (Alhamisi, Septemba 03, 2026) wakati akifungua Kongamano la Tano la Taifa la Ushiriki wa Watanzania katika Masuala ya Uchumi, lililofanyika Dodoma, lenye kaulimbiu inayosisitiza ushiriki wa Watanzania kama nguzo ya uchumi shindani na jumuishi kuelekea Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Amesema Serikali chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuweka mazingira ya kisera, kisheria na kiutendaji yatakayowawezesha Watanzania kushiriki moja kwa moja katika shughuli za kiuchumi, akisisitiza kuwa lengo si kuwazuia wawekezaji wa nje bali kuongeza uwezo na ushiriki wa Watanzania.

“Tuwawezeshe Watanzania kushika uchumi wao. Hii ndiyo njia ya kuongeza ajira, kuongeza vyanzo vya mapato na kujenga sekta binafsi yenye nguvu,” amesema.

Dkt. Mwigulu amesema Tanzania ina rasilimali nyingi na fursa kubwa za kiuchumi, hivyo ni muhimu kuhakikisha fursa hizo zinatafsiriwa kuwa ajira, biashara, uwekezaji na umiliki kwa Watanzania.Dkt. Mwigulu ameiagiza Wizara ya Fedha kuhakikisha marekebisho yanayofuata ya sheria za ununuzi yanaongeza wigo wa miradi inayoweza kutekelezwa na kampuni za Kitanzania.

Amesema kiwango cha Shilingi bilioni 50 kwa baadhi ya miradi kimekuwa kidogo kutokana na kukua kwa uchumi na uwezo wa kampuni za ndani, hivyo akapendekeza kiwango hicho kipandishwe hadi zaidi ya Shilingi bilioni 100 au Shilingi bilioni 150.

“Hii ya bilioni 50 imeshakuwa ya kawaida. Wekeni bilioni 100... au kama mnarekebisha sasa ikachukua muda, wekeni bilioni 150. Mambo yanaenda mbele. Tuwawezeshe Watanzania kushika uchumi wao,” amesema.

Amesisitiza pia kuwa fursa zinazotolewa na Serikali zinapaswa kutumiwa kwa uwajibikaji, akizitaka kampuni za Kitanzania kuhakikisha fedha za miradi zinatumika kutekeleza kazi kwa kiwango na ubora unaostahili, na kuonya kuwa Serikali haitasita kuchukua hatua dhidi ya watakaotumia vibaya fedha za umma.

Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu amezindua rasmi Mfumo wa Kitaifa wa Taarifa za Uwezeshaji Kiuchumi (NEMIS) unaolenga kurahisisha upatikanaji wa taarifa kuhusu fursa mbalimbali za uwezeshaji kwa Watanzania.

Mfumo huo utasaidia kuwafikishia wananchi taarifa kuhusu fursa za mitaji kupitia mifuko na programu za uwezeshaji, zabuni za umma, fursa za uwekezaji pamoja na taarifa nyingine muhimu za kiuchumi.Dkt. Mwigulu amehitimisha kwa kusisitiza umuhimu wa kuondoka kwenye mipango na sheria na kuelekea kwenye utekelezaji unaoleta matokeo kwa wananchi.

“Tanzania inasifika sana kwa mipango mizuri, inasifika sana kwa sheria hizi hizi tunazoziandika. Sasa tupige hatua twende kwenye kuhakikisha haya tunayotekeleza, haya tunayopanga, haya tunayoyaandika yanaonekana kwenye vitendo.”

Akizungumza katika kongamano hilo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Prof. Palamagamba Kabudi, amesema Serikali imeendelea kuweka mifumo, sera na sheria zinazolenga kuongeza ushiriki wa Watanzania katika uchumi, akisisitiza umuhimu wa uratibu ili fursa hizo ziwafikie wananchi na kuongeza ushiriki wao katika shughuli za kiuchumi.

Kwa upande wake, Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, amesema manunuzi ya bidhaa na huduma katika sekta ya madini yanafikia Shilingi trilioni 5.1 kwa mwaka, ambapo Serikali imehakikisha asilimia 90 ya manunuzi hayo yanabaki nchini Tanzania, hatua inayoongeza ushiriki wa Watanzania katika mnyororo wa thamani wa sekta hiyo.

Kwa niaba ya Bunge, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Edwin Swale, amesema Bunge limeendelea kuunga mkono hatua za Serikali za kuwawezesha wananchi kiuchumi kupitia maboresho ya sheria, akibainisha kuwa Serikali imeweka mifuko zaidi ya 74 ya uwezeshaji na imeendelea kuchukua hatua za kupunguza vikwazo kwa wafanyabiashara na wajasiriamali.

Nae, Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Uwezeshaji Kiuchumi, Prof. Aurelia Kamuzora, amesema uwezeshaji wa wananchi unapaswa kwenda sambamba na kujenga uwezo wa watu, upatikanaji wa mitaji, taarifa na ujuzi ili Watanzania waweze kushindana ndani na nje ya nchi.

Amesema Baraza limeweka mkazo katika kuwafikishia wananchi taarifa za fursa za kiuchumi na kuimarisha vituo vya uwezeshaji katika mikoa na wilaya.













-Yazindua bidhaa tatu za Jubilee Life Insurance ambazo ni Fanaka Plus, Smart Education Insurance Plan na Akiba Flex Plan


Na Said Mwishehe, Michuzi TV

MAMLAKA ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) imezitaka kampuni za bima kubuni bidhaa zinazotoa majibu ya vitendo kwa changamoto zinazowakabili wananchi, ikisema ubora wa bidhaa za bima haupaswi kupimwa kwa idadi ya watu waliojiunga pekee.

Kamishna wa Bima, Dk.Baghayo Saqware amesema kampuni zinazolenga kuongeza ujumuishi wa kifedha zinapaswa kwanza kuelewa mazingira wanamoishi Watanzania na changamoto zinazowakabili kabla ya kubuni bidhaa zinazokidhi mahitaji yao.

Dk.Saqware ametoa kauli hiyo katika hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Mkurugenzi wa Uzingatiaji wa Sheria na Kanuni wa TIRA, Bw Alex Rock wakati wa uzinduzi wa bidhaa tatu mpya za bima ya maisha za Jubilee Life Insurance Tanzania uliofanyika leo Septemba 3,2026 jijini Dar es Salaam.

“Mwito wangu kwa Jubilee Life Insurance na kampuni nyingine za bima ni kuendelea kubuni bidhaa zinazotoa majibu kwa changamoto za wananchi na kuboresha maisha yao,” amesema Dk Saqware.

“Ubora wa bidhaa haupimwi kwa idadi ya watu waliojiunga pekee. Uelewa hujenga imani, na imani huongeza matumizi endelevu ya bima,”amesema na kuongeza Tanzania inaingia katika hatua muhimu ya kujenga familia zenye uwezo wa kustahimili misukosuko ya kifedha na taifa lenye uimara wa kifedha huku bima ya maisha ikiwa na nafasi muhimu katika kulinda wananchi na kusaidia mipango yao ya muda mrefu.

Katika hafla hiyo, Dk.Saqware amezindua bidhaa tatu za Jubilee Life Insurance ambazo ni Fanaka Plus, Smart Education Insurance Plan na Akiba Flex Plan, zilizobuniwa kusaidia wananchi katika uwekaji akiba, maandalizi ya elimu, ulinzi wa maisha na mahitaji mengine ya kifedha ya baadaye.

Ameongeza Jubilee Life Insurance kwa kuwasilisha bidhaa hizo kwa lugha ya Kiswahili, akisema matumizi ya lugha inayoeleweka kwa urahisi ni muhimu katika kuongeza uelewa na ujumuishi katika huduma za bima.

“Matumizi ya lugha inayoeleweka katika kutoa taarifa na elimu kuhusu bima huwawezesha wananchi kuelewa kwa usahihi faida, masharti na wajibu wao kabla na baada ya kujiunga na bima,” alisema.

Dk.Saqware amesema pia bima ya maisha ni nyenzo muhimu katika kujenga usalama wa kifedha na uwezo wa kustahimili changamoto kwa mtu binafsi, familia na taifa kwa ujumla.

Amesisitiza bima hiyo hulinda kipato na mipango ya maisha dhidi ya athari za kifo, ulemavu, maradhi, ajali na matukio mengine yasiyotarajiwa, huku pia ikiwasaidia wananchi kuweka akiba kwa ajili ya mahitaji muhimu ya baadaye, yakiwemo elimu ya watoto na ustawi wa familia.

“Bila ulinzi wa bima, tukio lisilotarajiwa linaweza kukatisha elimu ya watoto, kuathiri maisha ya familia na hata kuzima ndoto za wanufaika,” alisema.Kupitia bima ya maisha, ndoto na mipango hiyo inaweza kulindwa na kuendelea kuwa halisi.”

Pia amesema matumizi ya bima ya maisha nchini bado hayajafikia kiwango kinachotarajiwa, huku baadhi ya sababu zikitajwa kuwa ni aina na muundo wa bidhaa zinazopatikana sokoni pamoja na uwezo wake wa kujibu mahitaji halisi ya wananchi.

Pamoja na hayo amesema uzinduzi wa bidhaa hizo unaendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kujenga uchumi imara, jumuishi na wenye uwezo wa kustahimili misukosuko.

Amesema hatua hiyo pia inaunga mkono Mpango Mkuu wa Maendeleo ya Sekta ya Fedha wa mwaka 2020–2030, ambao unalenga kuongeza mchango wa bima ya maisha katika pato la taifa hadi kufikia asilimia 3 ifikapo mwaka 2030.

Kwa upande wake Ofisa Mtendaji Mkuu wa Jubilee Life Insurance Tanzania Helena Mzena amesema kampuni hiyo imeendelea kuboresha bidhaa zake ili kuwapatia wateja thamani na uhakika zaidi.

Amesema Fanaka Life Plan imeboreshwa na kubadilishwa jina kuwa Fanaka Plus, ikiwapa wateja fursa ya kukuza fedha zao huku wakipata ulinzi wa maisha na amani ya moyo.

Ameongeza kuwa Akiba Flex inawapa wateja uhuru zaidi wa kuweka michango na kufanya miamala ya fedha kulingana na mahitaji yao.

Aidha, amesema Smart Education Insurance Plan imeundwa mahsusi kuwasaidia wazazi na walezi kujiandaa kwa ajili ya elimu ya watoto wao.“Hapa, mteja anaweza kuweka akiba ili kuhakikisha ndoto za kielimu za watoto wake zinatimia, huku pia akiwa na ulinzi wa maisha.

“Bidhaa hizi za bima ni ushahidi kwamba tunajali na kuthamini ndoto za wateja wetu na tunataka kuhakikisha ndoto hizo zinatimia bila msongo usio wa lazima.”

Wakati huo huo Mwenyekiti wa Bodi ya Jubilee Insurance Amyn Lalji amesema uzinduzi huo ni hatua nyingine muhimu katika safari ya Jubilee Life Insurance Tanzania na unaakisi dhamira ya kampuni hiyo ya kutoa suluhisho bunifu na la vitendo linalokidhi mahitaji yanayobadilika ya Watanzania.





Na Mwandishi Wetu

MAKAMU wa Rais wa Tanzania, Deogratius Ndejembi, ametoa maeekezo kwa Wizara ya Viwanda na Biashara kukaa meza moja na wazalishaji wa saruji nchini ili kuweka mikakati ya haraka itakayohakikisha saruji inapatikana kwa wingi na bei nafuu.

Ametoa maelekezo jijini Dar es Salaam alipokuwa katika hafla ya utoaji wa Tuzo za Rais kwa Mzalishaji Bora Viwandani (President’s Manufacturer of the Year Awards - PMAYA), zinazoratibiwa na Shirikisho la Wenye Viwanda Tanzania (CTI).

Akieleza kero ya wananchi kuhusu gharama za ujenzi, Makamu wa Rais amesema kwamba wananchi wanalazimika kununua saruji kwa bei kubwa kutokana na usimamizi na uratibu dhaifu wa uzalishaji viwandani, jambo ambalo linaenda kinyume na maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Kutokana na bei ya saruji kuwa juu Makamu wa Rais Ndejembi amesema” Nakuagiza Waziri wa Viwanda na Biashara, Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda pamoja na Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), kaeni mmalize hili suala ili mwananchi apate saruji kwa bei iliyokuwepo awali.

Amesisitiza baada ya Wizara hiyo kukaa anataka kupata ripoti kuhusu jambo hilo huku akiwataka wajadili na kisha mwandike ripoti ambayo itakabidhiwa kwa Rais Dk.Samia Suluhu Hassan.


Na Mwandishi Wetu.

Dar es Salaam, Septemba 3, 2026: Wananchi wamehimizwa kujitokeza kwa wingi kupigia kura kazi 294 za uandishi wa habari na makala za maendeleo zilizofuzu katika Samia Kalamu Awards 2026.

Wito huo umetolewa leo, Septemba 3, 2026, na Mwakilishi wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa habari (JAB) Prudence Constantine, wakati wa mkutano wa kutangaza kuanza kwa zoezi la upigaji kura litakalodumu hadi Septemba 30, 2026.

Prudence amesema kura za wananchi ni sehemu muhimu ya mchakato wa kumpata mshindi, kwa kuwa zinatoa nafasi kwa jamii kutambua na kuunga mkono kazi zilizoleta mchango au athari chanya katika maisha ya watu na maendeleo ya Taifa.

Amesema wananchi, wakiwa watumiaji wa maudhui ya habari, wana nafasi ya kuchagua kazi wanazoona zimefanya vizuri, zimeakisi mahitaji na maslahi ya jamii na kusaidia kuibua au kuelimisha kuhusu masuala muhimu ya maendeleo.

Wananchi wanaweza kupiga kura kupitia tovuti ya www.samiaawards.tz na kufuata maelekezo yaliyowekwa ili kuchagua kazi wanayoipendelea.

Pia, kura zinaweza kupigwa kupitia ujumbe mfupi wa maandishi kwa kutuma neno “SKA”, likifuatiwa na namba ya mshiriki kwenda 15200.

Akizungumza kuhusu Kazi 294 zilizofuzu kupigiwa kura Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Mhandishi Peter Mwasalyanda amesema kazi hizo zimefuzu baada ya tathmini ya kazi 3,003 zilizowasilishwa na waombaji 985. Jopo la majaji lilifanya tathmini kwa kuzingatia vigezo vilivyowekwa na kuteua kazi zilizopata alama za juu.

Naye Mwenyekiti Mwenza wa Mashindano hayo na Mkurugenzi wa TAMWA, Dkt. Rose Reuben, amesema mashindano hayo yamewaleta pamoja waandishi wa habari kutoka maeneo ya vijijini na mijini, akisisitiza kuwa washiriki watashindana kwa kuzingatia ubora wa kazi zao na si umaarufu wao.

Kwa mujibu wa mmoja wa majaji wa mashindano hayo, Bi. Beatrice Bandawe, amesema kuwa miongoni mwa maeneo yaliyopatiwa kipaumbele katika kazi zilizowasilishwa ni pamoja na afya, jinsia na makundi maalum, mazingira pamoja na elimu.

Samia Kalamu Awards zinaandaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA kwa Kuhsirikiana na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) pamoja na Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) zikilenga kutambua, kuenzi na kuhamasisha ubora, weledi na ubunifu katika uandishi wa habari na utayarishaji wa makala za maendeleo nchini.





VIJANA 50 wenye ufaulu wa juu lakini wanaotoka katika familia zenye uwezo mdogo wa kifedha watanufaika na uwezeshaji wa elimu ya chuo kikuu na maandalizi ya kuingia katika soko la ajira.

NMB Foundation (NMBF), ikishirikiana na Benki ya NMB, imetenga Sh bilioni 1 kuwawezesha vijana hao kupitia dirisha la tatu la programu ya Nuru Yangu Scholarship and Mentorship kwa mwaka wa masomo 2026/27.

Maombi yote yatapokelewa kupitia tovuti ya NMB Foundation, foundation.nmbbank.co.tz, kuanzia leo hadi tarehe 18 Septemba 2026.

Programu hiyo inalenga Watanzania waliomaliza Kidato cha Sita mwaka huu kwa Daraja la Kwanza lenye pointi tatu hadi tano. Waombaji pia wanapaswa kuwa na ushahidi wa uhitaji wa kifedha na kutarajia kujiunga na taasisi za elimu ya juu zinazotambuliwa nchini.

Akizungumza jijini Dar es Salaam, Meneja Mkuu wa NMB Foundation, Nelson Karumuna, alisema vijana watakaochaguliwa wataungana na wanufaika 101 waliowezeshwa kupitia awamu mbili zilizopita.

Kwa kuongezwa vijana hao 50, idadi ya wanufaika wa programu hiyo itafikia 151. NMBF imetumia zaidi ya Sh bilioni 2.1 katika awamu zilizopita, huku Sh bilioni 1 zikitengwa kwa kundi jipya.

“Uwezeshaji huu utagharamia ada, fedha za kujikimu, mafunzo kwa vitendo, malipo ya lazima ya chuo na vifaa vya kujifunzia, ikiwemo kompyuta mpakato,” alisema Karumuna.

Alisema vijana watakaopatikana pia watapatiwa malezi na ushauri wa kitaaluma, mafunzo ya uongozi, maandalizi ya kuingia katika soko la ajira na fursa za kujifunza kwa vitendo.

Karumuna alisisitiza kuwa maombi hayana gharama na hakuna mtu wala taasisi iliyopewa mamlaka ya kuuza nafasi hizo. Uchaguzi utafanywa kwa kuzingatia vigezo vilivyowekwa na uhakiki wa kina ili kuhakikisha fursa zinawafikia walengwa.

Programu ya Nuru Yangu ilianzishwa Mei 19, 2022, ikiwa na lengo la kuondoa vikwazo vya kifedha vinavyowazuia vijana wenye uwezo mkubwa kitaaluma kuendelea na elimu ya juu.

Mmoja wa wanufaika wake, Elia Johnson Kaberege, aliyehitimu Shahada ya Uhasibu katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mwaka 2025, alisema programu hiyo ilimwezesha kumudu gharama za masomo na mahitaji mengine ambayo familia yake isingeweza kugharamia.

Naye Irene John Busorwa, mhitimu wa Chuo Kikuu Mzumbe, alisema alikaribia kukosa nafasi ya kujiunga na chuo kutokana na hali ya kifedha ya familia yake. Kupitia Nuru Yangu, aliweza kusoma kwa miaka mitatu na kuhitimu. Kwa sasa ameajiriwa katika kampuni ya ukaguzi wa hesabu.

NMBF, ikishirikiana na Benki ya NMB, imewataka vijana wenye sifa kutuma maombi kupitia tovuti rasmi pekee kabla ya kufungwa kwa dirisha hilo Septemba 18, 2026.





Na mwandishi wetu

Makamu wa Rais Deogratius Ndejembi akimkabidhi tuzo Msemaji wa Kampuni ya Alliance One Wakili John Magoti(kulia), ambaye kampuni yake imetwaa nafasi ya Mshindi wa Pili wa Jumla wa Tuzo za Rais za Mzalishaji Bora wa mwaka pamoja na mshindi wa Kwanza wa Sekta ya Uchakataji Tumbaku, huku Waziri wa Viwanda na Biashara Wakili Judith Kapinga akishuhudia.

Makamu wa Rais Degratius Ndejembi amewaasa wazalishaji wa viwanda nchini kuhakikisha uzalishaji wa bidhaa nchini, unalenga kuwapunguzia mzigo wa gharama za maisha watanzania.

Amesema hayo kwenye hafla ya utoaji wa Tuzo za 19 za Rais za Wazalishaji bora za mwaka huu, ambapo Makamu wa Rais amemwakilisha Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan.Katika tuzo hizo kampuni ya tumbaku ya Alliance One, imekuwa kinara wa tuzo hizo kwa kushika nafasi ya mshindi wa pili wa jumla ya tuzo zote, lakini pia imeshinda tuzo ya mzalishaji bora wa uchakatataji tumbaku.
Akitoa mfano amesema wazalishaji wa simenti nchini wanapaswa kuongeza ushirikiano kata yao na wauza malighafi, ikiwemo klinka na malighafi nyingine, lengo likiwa kushusha gharama bidhaa hiyo, sambamba na maelekezo ya Rais kwamba wananchi waipate bidhaa hiyo kwa bei ya awali ambayo ilikuwa ni ndogo.

 “Katika kukuza uchumi na kuboresha maisha ya Watanzania, sekta ya viwanda ina nafasi kubwa sana,na duniani kote sekta ya viwanda ndiyo chimbuko la mandeleo ya haraka mhimiri mkuu wa uongezaji thamani wa malighafi zilizopo nchini na mtoaji wa ajira kwa wananchi na kuongeza mapato ya serikali pampja na fedha za kigeni,”amesema.

Ameipongeza kauli mbiu tuzo hizo mwaka huu ambayo ni kuhamasisha uendelevu,uwajibikaji na ustahimilivu katika uzalishaji viwandani, kwani inanenda sambamba na dira ya maendeleo ya taifa ya mwaka 2050 ikichagiza na kuchochea mageuzi endelevu ya viwanda hapa nchini.

 “Kutokana na wingi wa raslimali tulizonazo hapa nchini ikiwemo misitu na madini mbalimbali ni muhimu kukuza sekta ya viwandana kuendelea kujenga mahusiano na sekta ya viwanda na sekta nyingine ili kuongeza ufanisi na kuharakisha maendeleo jumuishi na hatimaye kuongeza kipato cha watanzania walio wengi,”amesema.

Amesema serikali za inatambua na kuunga mkono juhudi za sekta ya uzalishaji nchini, kwani kutokana na hilo, mchango wa sekta uzalishaji viwandani kwenye pato la taifa mwaka 2025 ulifikia asilimia 5.9 na pia asilimia 12 mpaka 22 ya bidhaa zilizouzwa nje ya nchi kwenye mwaka huo zilikuwa za viwandani.

Hata hivyo aliwaasa wenye viwanda nchini kuongeza uzalishaji hatimaye waweze kupenya na kukabiliana na ushindani kwenye masoko ya nchi jirani na siyo kuzalisha bidhaa za soko la hapa nchini peke yake.

Akiongea baada ya kupokea tuzo hiyo, Msemaji wa Alliance One Wakili John Magoti ameishukuru serikali ya awamu ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuweka mazingira mazuri ya kazi na biashara nchini yanayowezesha uwekezaji katika uzalishaji bora na endelevu.

“Sisi Alliance One tumeipokea tuzo hii kwa bashasha sana tukiamini kwamba imepatikana kutokana na uwajibikaji wa pamoja kati yetu sisi wafanyakazi wa kudumu wapatao 350 pamoja na wale msimu 4,600 na wadau wengine ambao ni wakulima wa tumbaku zaidi ya laki moja, na kiukweli tuzo hii ni yetu sote kwa pamoja,” amesema.

Amesema kampuni hiyo imeboresha uzalishaji ikiwemo matumizi ya umeme jua kiwandani nyakati za mchana na pamoja na matumizi ya gesi asilia kwenye magari na baadhi ya mitambo kiwandani hapo.

“Tumefanya hivyo ili kwenda sambamba na mdundo wa dunia ambao ni utunzaji wa mazingira na upunguzaji wa gesi ya ukaa wakati huo huo tukiongeza tija na kuokoa baadhi ya gharama ambazo sasa tunazirejesha kwa wananchi kama misaada kwa jamii ambapo kila mwaka tunatenga zaidi ya milioni 500 kusaidia jamii kwenye elimu,maji na mazingira,” amesema.

Washindi wengine wa Tuzo za 19 za Mzalishaji bora ni Sili Africa ambaye ni mshindi wa Jumla huku Kiwanda cha Sigara kikishika nafasi ya Tatukwenye tuzo hizo zinazoratibiwa na Shirikisho la wenye viwanda Tanzania (CTI).

Akongea kwenye hafla hiyo, Mwenyekiti wa CTI Sufian Ally ameiomba serikali kuongeza mapambano dhidi ya bidhaa bandia zinazoathiri soko la bidhaa za viwandani.

Aidha, ameiomba serikali kuendelea kuweka mazingira ya mazuri ya uzalishaji ikiwemo kupunguza gharama za uzalishaji kwa kutazama upya gharama za umeme,kumaliza tatizo la ucheleweshaji wa uondoaji bidhaa kutoka bandarini,pamoja na ushiriki wa kampuni za kitanzania kwenye tenda mbalimbali mambo ambayo Makamu wa Rais amesema serikali inaenda kuyafanyia kazi.

 




Na Mwandishi Wetu
OFISI ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR-TAMISEMI) imeanza kuwajengea uwezo walimu wa shule za sekondari za Serikali katika Jiji la Arusha na Halmashauri ya Arusha kuhusu matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika ufundishaji, ujifunzaji na upimaji wa wanafunzi.

Mafunzo hayo ya siku nne yanayofanyika katika Hoteli ya Gold Crest jijini Arusha kuanzia Septemba mosi hadi nne, 2026, yanafanyika kwa ushirikiano kati ya OR-TAMISEMI, Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) na Taasisi ya Elimu Tanzania (TIE).

Mafunzo hayo yanaendeshwa kupitia Mradi wa ICT Transforming Education in Africa – Awamu ya Tatu, unaoungwa mkono na Mfuko wa Korean Funds-in-Trust (KFIT), kwa lengo la kuwapatia walimu ujuzi wa vitendo wa kuunganisha TEHAMA katika ufundishaji, ujifunzaji na upimaji.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mkurugenzi Msaidizi wa Elimu kutoka OR-TAMISEMI, Melchiory Baltazary, alisema Serikali imejipanga kuendelea kuimarisha uwezo wa walimu kutumia TEHAMA kwa ufanisi ili kuboresha ubora wa elimu nchini.

Alisema ushirikiano kati ya Serikali, UNESCO na TIE umekuwa muhimu katika kuwapatia walimu ujuzi wa vitendo ambao wanaweza kuutumia moja kwa moja katika shughuli za ufundishaji na ujifunzaji.

Baltazary aliwataka walimu hao kutumia kikamilifu maarifa wanayoyapata na kuyasambaza kwa walimu wenzao ambao hawakupata nafasi ya kushiriki mafunzo hayo.

Alisema mfumo wa mafunzo wa kueneza ujuzi (cascade training) utasaidia kuwafikia walimu wengi zaidi katika shule na halmashauri zao.

Pia aliwahimiza walimu kuendelea kutumia mifumo na rasilimali za kidijitali zinazotolewa na Serikali ili kuimarisha uwezo wao kitaaluma hata baada ya kumalizika kwa mafunzo ya ana kwa ana.

Kwa upande wake, Mkuu wa Sekta ya Elimu katika Ofisi ya UNESCO Dar es Salaam, Dkt. Faith Shayo, alisema uimarishaji wa ujuzi wa kidijitali kwa walimu ni muhimu ili kuhakikisha mfumo wa elimu unaendana na kasi ya mabadiliko ya teknolojia.

Dkt. Shayo aliwataka walimu hao kushirikisha wenzao maarifa na ujuzi wanaoupata ili kuongeza idadi ya walimu wanaoweza kutumia TEHAMA katika elimu

Alisema walimu wana nafasi kubwa katika mabadiliko ya elimu kwa kuwa ndio wanaohakikisha teknolojia na ubunifu vinatafsirika kuwa mbinu bora za ufundishaji ndani ya madarasa.

“Tunatarajia mtashirikisha walimu wenzenu mnayojifunza hapa ili nao waweze kwenda sambamba na mabadiliko haya katika elimu,” alisema.

Aliongeza kuwa teknolojia inapaswa kutumika kuboresha ubora wa ufundishaji na ujifunzaji, kuongeza upatikanaji wa maarifa na kuwawezesha wanafunzi kupata ujuzi unaohitajika katika karne ya 21.

Naye Afisa Taaluma wa Mkoa wa Arusha, Oscar Kapinga, alisema matumizi sahihi ya teknolojia yanaweza kurahisisha ufundishaji na ujifunzaji pamoja na kuongeza fursa kwa wanafunzi kupata maarifa na rasilimali mbalimbali za kielimu.

Aliwataka walimu kuhakikisha matumizi ya TEHAMA yanaelekezwa katika maeneo yanayochangia moja kwa moja kuboresha matokeo ya ujifunzaji.

Mafunzo hayo yanahusisha maeneo mbalimbali ya ujuzi wa kidijitali, ikiwamo matumizi ya zana na majukwaa ya kujifunzia kidijitali, matumizi ya TEHAMA katika ufundishaji na upimaji, Rasilimali Huria za Kielimu (OER), utafutaji wa taarifa mtandaoni na matumizi ya teknolojia katika utekelezaji wa mtaala.

Pia walimu wanafundishwa mbinu shirikishi za ufundishaji, usimamizi wa kumbukumbu na taarifa za shule, uandaaji wa rasilimali za kujifunzia kidijitali, utengenezaji wa maudhui ya kielimu kwa njia ya sauti na picha pamoja na matumizi ya Akili Bandia (AI) katika elimu.

Walimu hao wanatumia mfumo wa TIE wa Mafunzo Endelevu ya Maendeleo ya Kitaaluma kwa Walimu (TCPD LMS), unaounganishwa na mfumo wa Serikali wa MEWAKA, kupata vifaa vya mafunzo na kukamilisha moduli mbalimbali.

Akieleza utekelezaji wa mradi huo, Gabriela Lucas kutoka Sekta ya Elimu ya UNESCO, alisema mpango huo unaolenga kujenga uwezo wa walimu kutumia teknolojia kwa ufanisi katika ufundishaji na ujifunzaji unatumia pia mifumo iliyopo ya Serikali katika kuwawezesha walimu kuendelea kujifunza.

Alisema UNESCO inalenga kuhakikisha kila mwalimu anakuwa na uwezo wa kutumia TEHAMA katika ufundishaji na ujifunzaji.

Kwa mujibu wa Lucas, mfumo wa ICT-CSTT una viwango mbalimbali vya umahiri vinavyowawezesha walimu kukuza ujuzi wao wa kidijitali hatua kwa hatua kulingana na kiwango walichonacho.

Alisema mfumo huo una jumla ya moduli 15, huku mafunzo ya Arusha yakilenga viwango vya Mwanzo na Kati vinavyohusisha moduli 10, pamoja na utangulizi wa moduli tano za kiwango cha Juu.

Alifafanua kuwa mradi huo unatumia mfumo wa mafunzo ya kueneza ujuzi ambapo walimu wanaopata mafunzo wanatarajiwa kuwafundisha wenzao katika shule zao.

Alisema mafunzo hayo yameanza Morogoro na sasa yanaendelea Arusha, huku mradi ukitekelezwa pia nchini Namibia na Uganda.

Naye mwezeshaji kutoka TIE, Watson Mtewele, alisema moduli zinazotumika katika mafunzo hayo zinapatikana kupitia mfumo wa maendeleo endelevu ya kitaaluma kwa walimu unaojulikana kama MEWAKA.

Alisema mfumo huo unawawezesha walimu kuendelea kujifunza na kuimarisha ujuzi wao wa kitaaluma hata baada ya kumaliza mafunzo ya ana kwa ana.

Jumla ya walimu 64 kutoka Jiji la Arusha na Halmashauri ya Arusha wanashiriki mafunzo hayo na wanatarajiwa kurejea shuleni kwao na kuwasaidia walimu wenzao kutumia zana na majukwaa ya kidijitali, kuandaa maudhui ya kielimu na kutumia teknolojia katika ufundishaji, ujifunzaji na upimaji.

Mpango huo unalenga kujenga mtandao mpana wa walimu wenye ujuzi wa kidijitali kupitia mfumo wa kushirikishana na kuhamishiana maarifa na ujuzi, hatua inayotarajiwa kuwafaidisha wanafunzi.

Mafunzo hayo pia yanaunga mkono jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika elimu na kujenga nguvu kazi yenye ujuzi na maarifa yanayokidhi mahitaji ya karne ya 21.

Aidha, mpango huo unaendana na Dira ya Maendeleo ya Tanzania 2050 inayosisitiza umuhimu wa kuwa na wananchi wenye maarifa, ujuzi na uwezo wa kutumia teknolojia katika kuchochea maendeleo ya taifa.

Mafunzo hayo yanaendelea katika Hoteli ya Gold Crest jijini Arusha na yanatarajiwa kuhitimishwa Septemba 4, 2026.




Na Mwandishi Wetu
USHIRIKIANO kati ya Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) na Taasisi ya Zanzibar ya Uhasibu, Ukaguzi na Ushauri wa Kodi (ZIAAT) unatarajiwa kuongeza fursa za mafunzo, kuimarisha weledi wa wataalamu na kuchangia usimamizi bora wa fedha na huduma kwa umma.

Taasisi hizo zimetia saini Hati ya Makubaliano ya Ushirikiano (MoU) leo, Septemba 1, 2026, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa kitaaluma na kitaalamu. Akizungumza katika hafla hiyo, Afisa Mtendaji Mkuu wa TIA, Prof. William A. Pallangyo, amesema ushirikiano huo utawezesha taasisi hizo kutumia kwa pamoja utaalamu na rasilimali katika kuendeleza wataalamu.

Maeneo ya ushirikiano ni pamoja na mafunzo ya Certified Tax Technician (CTT), Maendeleo Endelevu ya Kitaaluma (CPD), usimamizi wa vituo vya mitihani vya CTT na CTP, tafiti, machapisho na mikutano ya kitaaluma, pamoja na kujenga uwezo wa wataalamu wa sekta ya fedha na utumishi wa umma.

Kwa wananchi na wataalamu, ushirikiano huo unatarajiwa kuongeza fursa za mafunzo na maendeleo ya kitaaluma, kukuza wataalamu wenye ujuzi na weledi zaidi, pamoja na kuibua tafiti na maarifa yatakayosaidia kutatua changamoto za jamii.

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa ZIAAT, CPA Ame Burhan Shadhil, ameipongeza TIA kwa kuweka mazingira bora ya kujifunzia na kuahidi kuendelea kushirikiana katika kuendeleza wahasibu, wakaguzi na watafiti. Amesema ushirikiano huo utasaidia kuimarisha weledi na uadilifu wa wataalamu na watumishi wa umma.

Kwa ujumla, makubaliano hayo yanaweka msingi wa kujenga nguvu kazi yenye ujuzi, weledi na uadilifu zaidi, kuimarisha usimamizi wa rasilimali na kuchangia utoaji wa huduma bora kwa wananchi, sambamba na juhudi za kufikia Dira ya Taifa 2050.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Deogratius Ndejembi amemwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika hafla ya utoaji wa tuzo za 19 za Rais za Wazalishaji Bora Viwandani, hafla iliyofanyika katika ukumbi wa Super Dome, Masaki Jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika hafla hiyo, Makamu wa Rais ametoa wito kwa Wizara ya Viwanda na Biashara kwa kushirikiana na wazalishaji wa saruji nchini, kuhakikisha wanatafuta suluhu ya haraka ili kurejesha bei ya kawaida ya saruji kwa wananchi. Amesema maono ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuona wananchi wanaweza kununua mfuko wa saruji kwa gharama nafuu hivyo ni lazima kuoanisha uzalishaji wa malighafi zote zinazochangia katika uzalishaji wa saruji ili bidhaa hiyo ipatikane kwa urahisi.

Halikadhalika, Makamu wa Rais amesema ni muhimu kufanya tathimini ya ukuaji wa viwanda hapa nchini ili kutambua ukuaji huo kama unaviwezesha viwanda kuwa na ushindani wa masoko katika kanda, Afrika na Dunia kwa ujumla.

Makamu wa Rais amesema Serikali itaendelea kuchukua hatua kali za kisheria kwa wafanyabishaara wote wanaojihusisha na biashara haramu za uingizaji bidhaa bandia ambazo hukwepa kodi na tozo mbalimbali stahiki ambapo, zinaathiri ukuaji wa viwanda, kusababisha upotevu wa mapato ya serikali pamoja na kupunguza ushindani wa bidhaa zinazozalishwa ndani ya nchi.

Amewataka wazalishaji wa viwandani hapa nchini, kufanya jitihada za kuongeza uchakataji wa malighafi ndani ya nchi kwa kuhakikisha wanaongeza thamani, hatua itakayosaidia katika kuongeza ajira kwa watanzania na ukuaji wa uchumi kwa kasi.

Aidha, Makamu wa Rais ameitaka Wizara ya Viwanda na Biashara kuhakiki takwimu sahihi za idadi ya viwanda vilivyopo ili kuweka mikakati ya namna ya kuongeza wanachama wa Shirikisho la Viwanda Tanzania, hali itakayorahisisha uwepo wa chombo kimoja kinachowawakilisha wazalishaji wa viwandani.

Makamu wa Rais amesema katika kukuza uchumi na kuboresha maisha ya watanzania, sekta ya viwanda ina nafasi kubwa kwa kuwa ndiyo chimbuko la maendeleo ya haraka na ni muhimili mkuu katika uongezaji thamani wa malighafi zilizopo, utoaji ajira kwa wananchi, kuongeza mapato ya Serikali pamoja na fedha za kigeni. Pia, amesema sekta ya viwanda ni muhimu katika kuboresha sayansi na teknolojia na kuongeza uzalishaji, na hivyo kukuza ubunifu, uvumbuzi, uchumi, na kuondoa umasikini nchini.

Amesema kutokana na wingi wa rasilimali zilizopo nchini ikiwemo misitu na madini mbalimbali, ni muhimu kukuza sekta ya viwanda na kuendelea kujenga mahusiano kati ya sekta ya viwanda na nyingine ili kuongeza ufanisi, kuharakisha maendeleo jumuishi na hatimaye kuongeza kipato cha Watanzania walio wengi.

Makamu wa Rais amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan itaendelea kufanya kazi kwa karibu na sekta binafsi ili kuharakisha maendeleo ya Taifa.

Kwa upande wake Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Judith Kapinga, amesema Wizara hiyo imeendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ili kuhakikisha lengo lake la kuendeleza sekta ya viwanda linafanikiwa. Amesema Sekta hiyo imeendelea kujiimarisha ili kuongeza nafasi katika mchango wa pato la Taifa na kuongeza ufanisi kwa lengo la ukuaji wa sekta hiyo muhimu.

Amesema tayari Wizara imekamilisha na itazindua Sera ya Maendeleo endelevu ya Viwanda ya Mwaka 2025 na Sera ya Maendeleo ya jasiriamali ndogo na za kati ya mwaka 2003 Toleo la mwaka 2025 ikiwa na lengo la kwenda sambamba na Dira 2050 ambayo inategemea uendelevu wa Viwanda.

Mwenyekiti wa Shirikisho la Viwanda Tanzania (CTI) Hussein Suphian Ally ameipongeza Serikali kwa mafanikio mbalimbali yanayoendelea kuimarisha mchango wa sekta ya viwanda nchini ikiwemo uwekezaji mkubwa unaofanywa katika miradi ya kimkakati ambayo imeendelea kuongeza ushindani katika sekta ya viwanda.

Amesema CTI inapongeza juhudi za Serikali za kuendelea na ujenzi wa miradi ya Reli ya Kisasa (SGR), ujenzi na upanuzi wa Bandari, ujenzi wa mitandao ya barabara pamoja na uwekezaji katika nishati na miundombinu mingine ya kiuchumi ambayo kwa pamoja imeendelea kupunguza gharama za usafirishaji, kurahisisha biashara na kuongeza uwezo wa bidhaa zinazozalishwa nchini kufikia masoko ya ndani, kikanda na kimataifa.

Katika hafla hiyo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amezawadia tuzo ya heshima kwa kutambua mchango wake katika uboreshaji wa mazingira ya uwekezaji na viwanda nchini.

Hafla hiyo imewakutanisha wazalishaji wakubwa, wakati na wadogo, wafanyabiashara pamoja na wadau wengine wa sekta ya viwanda na biashara, huku tuzo hizo zikiendelea kuwa jukwaa la kuhamasisha ubora, ubunifu, uwekezaji, matumizi ya teknolojia na uzalishaji endelevu nchini.







Na Mwandishi Wetu.
TANZANIA imefungua ukurasa mpya wa ushirikiano katika sayansi, teknolojia na ubunifu baada ya Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) kuingia katika ushirikiano na Kongani ya Ubunifu ya Incheon (Incheon Innovation Cluster—IIC) ya Korea Kusini.

Ushirikiano huo unalenga kuanzisha Tawi la IIC nchini Tanzania, hatua inayotarajiwa kuwaunganisha watafiti na wabunifu wa Tanzania na fursa za utaalamu, teknolojia, utafiti na biashara kutoka Korea Kusini.

Hafla ya utiaji saini wa Mkataba wa Makubaliano kati ya COSTECH na IIC imefanyika leo Septemba 3, 2026, katika Songdo Convensia, Incheon, Korea Kusini, ikiwa sehemu ya Mkutano wa Kimataifa wa Teknolojia za Mazingira wa Incheon 2026.

Akizungumza katika hafla hiyo, Balozi wa Tanzania nchini Korea Kusini, Noel Kaganda, alisema ushirikiano huo unapaswa kwenda zaidi ya Tanzania kupokea teknolojia kutoka nje.

“Tunapaswa kuachana na utamaduni wa kununua teknolojia zilizotengenezwa tayari na badala yake kuelekea katika kuzalisha teknolojia kwa pamoja, kuzijaribu kwa kuzingatia mazingira yetu na kuhakikisha zinaendana na mahitaji yetu,” alisema.

Kaganda alisema ubunifu unapaswa kuwa wa pande zote mbili, huku akisisitiza umuhimu wa Tanzania kushiriki katika mchakato wa kutengeneza na kuendeleza teknolojia.

“Ubunifu lazima uwe shirikishi. Hatupaswi kuwa na nchi moja inayozalisha na nyingine inayobaki kuwa mtumiaji pekee katika ikolojia ya ubunifu,” alisema.

Kupitia ushirikiano huo, watafiti na wabunifu wa Tanzania watapata nafasi ya kushirikiana na taasisi za utafiti, wataalamu na kampuni za Korea Kusini katika kuendeleza teknolojia na kuzifikisha katika matumizi ya kibiashara.

Mkataba huo unaainisha maeneo ya utafiti wa pamoja, maendeleo na uhamishaji wa teknolojia, ubunifu, ubia wa kibiashara pamoja na mikutano na programu za pamoja.

Fursa hiyo inatajwa kuwa muhimu kwa wabunifu ambao wamekuwa wakikabiliwa na changamoto ya kupeleka bunifu zao kutoka hatua ya wazo au mfano wa bidhaa hadi katika uzalishaji na soko.

Kwa upande mwingine, Korea Kusini itapata fursa ya kushirikiana na Tanzania katika kuelewa changamoto za ndani, ubunifu unaozalishwa nchini na fursa zilizopo katika soko la Tanzania na Afrika.

Akizungumzia umuhimu wa hatua hiyo, Kaganda alisema ushirikiano huo unaweza pia kuwa sehemu ya diplomasia ya sayansi, teknolojia na ubunifu kati ya Tanzania na Korea Kusini.

“Leo tunashuhudia utiaji saini wa Mkataba wa Makubaliano kati ya COSTECH na IIC. Huu ni ushahidi wa dhamira thabiti ya Serikali zetu katika kujenga diplomasia ya sayansi, teknolojia na ubunifu. Niwatake COSTECH na IIC kuendeleza diplomasia hii ya sayansi, teknolojia na ubunifu ili ushirikiano huu uweze kuleta matokeo yaliyokusudiwa kwa kiwango kikubwa,” alisema.

Ushirikiano huo pia unakuja wakati Serikali ya Tanzania ikisisitiza umuhimu wa kujifunza kutokana na uzoefu wa Korea Kusini katika kutumia sayansi, teknolojia na ubunifu katika kujenga uchumi.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, alitoa msukumo huo Julai 2, 2026, wakati wa uzinduzi wa shughuli za miaka 40 ya COSTECH, akitaka Tanzania kujifunza namna Korea Kusini ilivyotumia teknolojia na ubunifu katika mabadiliko yake ya kiuchumi.

Kwa wabunifu wa Tanzania, hatua hiyo sasa inaweka mezani swali la muhimu: ni bunifu zipi za Tanzania zitakazovuka mipaka na kupata nafasi katika mfumo wa teknolojia wa Korea Kusini?

Jibu lake litategemea uwezo wa COSTECH na IIC kubadili makubaliano hayo kuwa miradi halisi, utafiti wa pamoja, mafunzo, uhamishaji wa teknolojia, ubia wa biashara na fursa za soko kwa wabunifu wa Tanzania.

Hapo ndipo thamani halisi ya Tawi la IIC nchini Tanzania itakapopimwa.





Top News