Wataalam kutoka Makumbusho ya Taifa la Tanzania wametoa mafunzo ya kizalendo kwa washiriki wa shindano la Urembo wa Dunia, Tanzania (Miss World Tanzania 2026) katika ukumbi wa White Sand Resort, tarehe 16/04/2026 ikiwa ni sehemu ya kuwajengea uelewa kuhusu Utalii, historia, utamaduni na urithi wa Taifa.

Katika mafunzo hayo, mada mbalimbali ziliwasilishwa na wakufunzi hao kwa lengo la kuwawezesha washiriki kuitambua historia yao na kuwa mabalozi bora wa utamaduni wa Tanzania ndani na nje ya nchi.

Afisa Utalii, Bw. Chance Ezekiel aliwasilisha mada kuhusu Utalii wa Tanzania, akieleza kwa kina hatua za maendeleo ya sekta hiyo na kutoa mwelekeo wa kitaifa kuhusiana na tasnia nzima ya utalii na ubalozi wake hapa Tanzania.

Kwa upande wa Wahifadhi Historia, Bw. Nasri Omari alitoa mada kuhusu historia ya Makumbusho ya Taifa kwa kutolea ufafanuzi wa mamlaka na maeneo ya kiutawa ya taasisi pamoja na vituo na Malikale zinazosimamiwa nayo. Naye Bw. Shomari Rajabu alijikita katika kuelezea maadili, mila na namna bora ya kuzungumza na jamii ili kuendeleza na kulenga kuwa mabalozi bora wa Tanzania.

Washiriki wa Miss World Tanzania 2026 walionesha kufurahishwa na mafunzo hayo, wakibainisha kuwa yameongeza maarifa na uelewa wao kuhusu Utalii, historia, mila na desturi za Mtanzania.

Makumbusho ya Taifa inaendelea kutekeleza jukumu lake la kutoa elimu kwa umma kuhusu uhifadhi na uendelezaji wa urithi wa taifa kupitia programu mbalimbali za elimu na mafunzo.








Na Joseph Mahumi, WF, Washington D.C, Marekani
Tanzania imejipanga kikamilifu kuwa kitovu cha uwekezaji barani Afrika na inawakaribisha wawekezaji wa Marekani kuchangamkia fursa lukuki zilizopo katika sekta mbalimbali za uchumi.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) wakati alipoongoza ujumbe wa Tanzania katika Mkutano wa Uwekezaji ulioandaliwa na Baraza la Biashara la Kimataifa- Business Council for International Understanding (BCIU), uliofanyika katika Ofisi za BCIU, jijini Washington D.C nchini Marekani, pembezoni mwa Mikutano ya Majira ya Kipupwe ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF.

Mhe. Balozi Omar alieleza kuwa, Tanzania inaendelea kuimarika kiuchumi na kutoa mazingira rafiki kwa biashara na uwekezaji sambamba na uchumi wake kuendelea kukua kwa kasi, ukifikia asilimia 5.5 mwaka 2024 na unatarajiwa kufikia asilimia 6.0 mwaka 2025, hali inayochochewa na sekta muhimu kama kilimo, viwanda, madini, ujenzi pamoja na huduma za kifedha.

“Serikali inaendelea kuboresha mazingira ya biashara na kuvutia uwekezaji wa muda mrefu ili kuhakikisha sekta binafsi inachukua nafasi yake kikamilifu katika kukuza uchumi” alisema Mhe. Balozi Omar.

Aliongeza kuwa mahusiano ya kibiashara kati ya Tanzania na Marekani yanaendelea kuimarika kwa kasi, ambapo thamani ya biashara kati ya nchi hizo imefikia dola za Marekani bilioni 1.4 mwaka 2024 huku uwekezaji wa moja kwa moja kutoka Marekani umeongezeka kutoka dola milioni 12.3 mwaka 2020 hadi dola milioni 40 mwaka 2023.

Akifafanua fursa zilizopo, Mhe. Balozi Omar alisema Tanzania ina utajiri mkubwa wa madini muhimu kwa nishati safi kama graphite, nickel na madini adimu, huku akisisitiza kuwa nchi inakaribisha ubia wa kuongeza thamani badala ya kuuza malighafi pekee.

“Hatupendelei kuuza mawe ghafi, bali tunakaribisha ushirikiano wa kuanzia uchimbaji hadi uzalishaji wa bidhaa za mwisho zenye thamani kubwa, na Tanzania ina soko kubwa la vijana wanaohitaji huduma za kidijitali, hivyo ni fursa adhimu kwa wawekezaji wa teknolojia pia,” alisema Mhe. Balozi Omar.

Aidha, alisema kuwa katika sekta ya kilimo, Tanzania inalenga kuwa ghala la chakula kwa Afrika na dunia, akihimiza uwekezaji katika kilimo cha kisasa na usindikaji wa mazao. Pia alieleza kuwa sekta ya afya, miundombinu na maeneo maalum ya uwekezaji (SEZs) yana fursa kubwa kutokana na mahitaji makubwa ya soko la ndani na kikanda.

Naye Balozi wa Tanzania nchini Marekani, Mhe. Dkt. Elsie Sia Kanza alisema kuwa mkutano huo na wawekezaji wa Marekani ni jitihada za kuvutia zaidi mitaji kutoka Marekani kupitia Diplomasia ya kiuchumi.

Alisema kuwa Tanzania inaanza kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 ambayo imeelekeza nchi iweze kufikia uchumi wa dola za Marekani trilioni 1 ifikapo Mwaka 2050 na kwamba uwekezaji wa Sekta Binafsi unatarajiwa kuwa na mchango mkubwa.

Kwa upande wa wawekezaji walioshiriki mkutano huo ulioongozwa na Rais na Afisa Mtendaji Mkuu wa Baraza la Biashara - Business Council for International Understanding (BCIU), Bw. Peter Tichansky, walisema wameona kuna fursa za kiuchumi nchini Tanzania na wamejipanga kuwekeza katika sekta muhimu ikiwemo kilimo, madini, afya, miundombinu ya bandari, Teknolojia ya Habari na Mawasiliano pamoja na Bima ya wakulima.

Walisema kuwa eneo pamoja na maeneo hayo mengine, wanataka kuwekeza katika kilimo kwa kuzalisha mbegu bora pamoja na kuwawekea wakulima bima ya kilimo ili wawe na uhakika wa kuendesha shughuli zao bila kupata hasara ya majanga yatokanayo na changamoto mbalimbali.


Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akizungumza jambo wakati wa MKutano wa Uwekezaji ulioandaliwa na Baraza la Biashara - Business Council for International Understanding (BCIU), uliofanyika katika Ofisi za BCIU, jijini Washington D.C nchini Marekani, pembezoni mwa Mikutano ya Majira ya Kipupwe ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF, ambapo BCIU wameonesha nia kuwekeza nchini katika Bima kwa wakulima, kuzalisha mbegu bora za kisasa, bandari na katika Sekta ya Afya.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb)(kushoto), akiwa na Rais na Afisa Mtendaji Mkuu wa Baraza la Biashara - Business Council for International Understanding (BCIU), Bw. Peter Tichansky, baada ya Mkutano wao wa Uwekezaji ulioandaliwa na Baraza la Biashara - Business Council for International Understanding (BCIU), uliofanyika katika Ofisi za BCIU, jijini Washington D.C nchini Marekani, pembezoni mwa Mikutano ya Majira ya Kipupwe ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF, ambapo BCIU wameonesha nia kuwekeza nchini katika Bima kwa wakulima, kuzalisha mbegu bora za kisasa, bandari na katika Sekta ya Afya.
Ujumbe wa Tanzania ukiongozwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (kulia), ukiwa katika Mkutano wa Uwekezaji ulioandaliwa na Ujumbe Baraza la Biashara - Business Council for International Understanding (BCIU) (kushoto), uliofanyika katika Ofisi za BCIU, jijini Washington D.C nchini Marekani, pembezoni mwa Mikutano ya Majira ya Kipupwe ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF, ambapo BCIU wameonesha nia kuwekeza nchini katika Bima kwa wakulima, kuzalisha mbegu bora za kisasa, bandari na katika Sekta ya Afya.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (Katikati), Rais na Afisa Mtendaji Mkuu wa Baraza la Biashara - Business Council for International Understanding (BCIU), Bw. Peter Tichansky (wa tatu kulia), Balozi wa Tanzania nchini Marekani, Mhe. Elsie Sia Kanza (wa pili kulia), Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Mipango ambaye pia ni Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt. Tausi Kida (wa pili kushoto), Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango Zanzibar, Bw. Aboud Hassan Mwinyi (wa tatu kushoto), na viongozi wengine wa BCIU, Bw. Mathias Berninger (wa kwanza kulia) na Bi. Mesiya Mwangoka (kushoto), wakiwa katika picha ya pamoja baada ya MKutano wa Uwekezaji ulioandaliwa na Baraza la Biashara - Business Council for International Understanding (BCIU), uliofanyika katika Ofisi za BCIU, jijini Washington D.C nchini Marekani, pembezoni mwa Mikutano ya Majira ya Kipupwe ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF, ambapo BCIU wameonesha nia kuwekeza nchini katika Bima kwa wakulima, kuzalisha mbegu bora za kisasa, bandari na katika Sekta ya Afya.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Washington D.C, Marekani)

Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Serikali ya Tanzania kupitia Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA) imeweka mkazo katika kuimarisha usalama wa mifumo ya TEHAMA, kuongeza ufanisi wa huduma za kidijitali pamoja na kuunganisha mifumo ya taasisi za umma ili kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Akizungumza Bungeni jijini Dodoma Aprili 17, 2026, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani J. Kikwete, alisema hatua hizo ni sehemu ya mpango wa maboresho ya huduma za serikali kwa mwaka wa fedha 2026/27.

Waziri Kikwete alieleza kuwa katika kipindi hicho, e-GA itafanya tathmini ya usalama wa mifumo na miundombinu ya TEHAMA katika taasisi 571 za umma ili kuhakikisha mifumo hiyo inafanya kazi kwa ufanisi, uimara na usalama wa hali ya juu.

Aidha, Serikali inalenga kuboresha na kuunganisha mifumo jumuishi ya TEHAMA pamoja na mifumo ya kisekta na ya kitaasisi, lengo likiwa ni kupunguza urudufu wa mifumo na kuongeza ushirikiano kati ya taasisi za serikali.

Katika hatua nyingine, e-GA itahusika katika kuchambua, kubuni na kuendeleza mifumo mipya ya kisekta kwa taasisi mbalimbali, ili kurahisisha utoaji huduma na kuongeza ufanisi wa kiutendaji ndani ya serikali.

Serikali pia imepanga kuunganisha taasisi zote za umma kupitia Mfumo wa Kubadilishana Taarifa Serikalini (GovESB), hatua itakayorahisisha mawasiliano na ushirikiano wa kidijitali kati ya taasisi.

Vilevile, juhudi zitaelekezwa katika kuimarisha tafiti na ubunifu wa teknolojia mpya za TEHAMA ili kuibua huduma bora zaidi kwa wananchi, sambamba na kuhakikisha matumizi salama ya teknolojia zinazoendelea kujitokeza duniani.

Katika kuboresha upatikanaji wa huduma, mtandao wa mawasiliano wa Serikali utapanuliwa hadi kufikia wilaya zote nchini, huku mifumo kama e-Office na huduma nyingine za kidijitali ikiendelea kuboreshwa.

Kwa upande wa miundombinu, e-GA itaendelea kusimamia vituo vya kuhifadhi data za Serikali pamoja na mifumo ya ulinzi dhidi ya majanga ya kimtandao ili kuhakikisha taarifa za serikali zinalindwa wakati wote.

Aidha, Serikali itatoa mafunzo kwa watumishi wa umma na watumiaji wa mifumo ya TEHAMA ili kuongeza uelewa na ufanisi katika matumizi ya teknolojia katika utumishi wa umma.

Kwa ujumla, maboresho hayo yanalenga kuimarisha utawala bora wa kidijitali, kupunguza gharama za uendeshaji wa serikali na kuongeza kasi ya utoaji wa huduma bora kwa wananchi.




Na Mwandishi Wetu
SHIRIKA la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO) limetoa limesisitiza kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kulinda urithi wa mila, utamaduni, tiba asili na mazingira kama nguzo muhimu ya maendeleo endelevu ya Taifa.

TRAMEPRO inasisitiza kuwa maeneo ya mila, maarifa ya tiba asili, pamoja na mifumo ya jadi ya uhifadhi wa mazingira ni sehemu muhimu ya utambulisho wa jamii zetu. Taarifa iliyotolewa leo Aprili 17,2026 kwa vyombo vya habari na Katibu Mkuu

Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO) Boniventura Mwalongo, amesema kumekuwepo na changamoto za uvamizi wa maeneo ya mila, mabadiliko holela ya matumizi ya ardhi, pamoja na kuongezeka kwa upotoshaji wa dhana ya tiba asili.

“Mwito kwa Wazee na Machifu wa Mila

TRAMEPRO inatoa wito kwa viongozi wa mila kuendelea kusimamia kwa uaminifu maeneo ya jadi, kulinda urithi wa mababu, na kuendeleza maarifa ya tiba asili. Ushirikiano na Serikali na taasisi husika ni muhimu katika kuhakikisha amani na mshikamano wa kijamii unadumishwa.

Wito kwa Jamii kwa Ujumla

“Wananchi wote wanahimizwa kuthamini urithi wa kitamaduni, kuachana na imani potofu zinazokwamisha maendeleo, na kuzingatia sheria na miongozo rasmi. Umoja na uwajibikaji ni msingi wa ustawi wa Taifa.”

Aidha ametoa ombi kwa Serikali na Wadau wa Maendeleo kuviwezesha na kuviimarisha vikundi vinavyoendeleza tiba asili, utamaduni na uhifadhi wa mazingira, Kuimarisha ushirikiano wa tafiti kati ya taasisi za ndani na za kimataifa na Kusimamia kikamilifu utekelezaji wa sheria za ardhi na utamaduni

Pia kuchukua hatua dhidi ya vitendo vinavyosababisha migogoro ya kijamii na uvunjifu wa amani.

“Nukuu ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania , Kuhusu Mazingira na Utamaduni

“Tunapaswa kuthamini na kulinda mila zetu njema pamoja na mazingira yetu, kwa sababu hayo ndiyo msingi wa maendeleo endelevu ya Taifa letu.”

“Pia Shirika linamkumbuka kiongozi mashuhuri wa dunia, Benjamin Franklin, aliyezaliwa tarehe 17 Aprili 1706. Alikuwa mfano wa maarifa, ubunifu na maadili mema, akisisitiza umuhimu wa elimu, nidhamu na hekima katika kujenga jamii imara,” amesema Mwalongo,

Aidha amesema TRAMEPRO inawahimiza wananchi wote kushirikiana katika kulinda urithi wa utamaduni, kuendeleza tiba asili kwa misingi ya sayansi na teknolojia, pamoja na kuhifadhi mazingira kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.



Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Serikali ya Tanzania imeendelea kuimarisha mapinduzi ya kidigitali katika utoaji wa huduma kwa wananchi kupitia uwekezaji mkubwa katika Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), hatua inayolenga kuongeza ufanisi, uwazi na kupunguza urasimu katika taasisi za umma.

Akizungumza bungeni jijini Dodoma leo  Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete, amesema Serikali imechukua hatua za makusudi kuhakikisha huduma zinapatikana kwa haraka na kwa njia rahisi zaidi kupitia mifumo ya kidigitali.

Amesema katika kipindi cha kuanzia Julai 2025 hadi Machi 2026, jumla ya mifumo 252 ya serikali imeunganishwa katika mtandao mmoja wa kidigitali unaowezesha ushirikiano kati ya taasisi mbalimbali za umma.

Kwa mujibu wa Ridhiwani, hatua hiyo imeiwezesha serikali kuimarisha utoaji wa huduma kwa wananchi bila ulazima wa kufika ofisini, jambo ambalo limepunguza msongamano na kuongeza ufanisi katika utendaji wa kazi za umma.

Aidha, amesema mabadiliko hayo yameleta nafuu kubwa kwa wananchi kwa kupunguza muda na gharama walizokuwa wakitumia kufuata huduma mbalimbali za serikali, ambazo sasa zinapatikana kwa njia ya mtandao.

Waziri huyo amesema kuwa maboresho hayo pia yamechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza urasimu uliokuwa ukikwamisha upatikanaji wa huduma, hususan katika taasisi ambazo zilitegemea zaidi mifumo ya karatasi.

Ameongeza kuwa kuunganishwa kwa mifumo hiyo ya TEHAMA kumeongeza uwazi katika utendaji wa kazi za serikali, kwani taarifa sasa zinapatikana kwa urahisi na zinaweza kufuatiliwa kwa wakati halisi.

Ridhiwani amesema uwazi huo umeimarisha pia uwajibikaji ndani ya taasisi za umma, kwani kila hatua ya utoaji huduma inaweza kufuatiliwa na kudhibitiwa kupitia mifumo ya kidigitali.

Aidha, amesisitiza kuwa serikali itaendelea kuwekeza katika miundombinu ya TEHAMA na kuboresha mifumo iliyopo ili kuhakikisha huduma za umma zinakuwa za kisasa zaidi na zinakidhi mahitaji ya wananchi.

Amesema lengo la serikali ni kuhakikisha Tanzania inakwenda sambamba na mabadiliko ya teknolojia duniani, huku ikiboresha utoaji wa huduma za kijamii na kiuchumi kupitia mifumo ya kidigitali yenye ufanisi mkubwa.

Serikali imeeleza kuwa mageuzi hayo ni sehemu ya mkakati mpana wa kuimarisha utawala bora na kuongeza tija katika sekta ya umma, ikiwa ni pamoja na kupunguza mianya ya upotevu wa rasilimali na kuongeza uwajibikaji.



Maofisa wawili wa wakala wa misitu Tanzania (TFS) wilaya ya Makete mkoani Njombe wamehukumiwa Kifungo cha miaka miwili jela ama kulipa faini ya shilingi laki tano kila mmoja baada ya kukutwa na hatia ya kuomba na kupokea rushwa ya shilingi milioni 8 kwa Yuda Male mkazi wa kijiji cha Mfumbi kata ya Mfumbi wilayani hapo ambaye ni mfugaji baada ya kuingiza mifugo katika Msitu wa asili wa serikali wa Chimala. 

Akitoa hukumu katika mahakama ya wilaya ya Makete Aprili 16, 2026 Hakimu mkazi Mfawidhi Mwandamizi mahakama hiyo Irvan Msacky amesema mshitakiwa Thadeus James Mtui(31) mhifadhi TFS Matamba na  Florian Giliad Kilango(33) afisa wa TFS wilaya ya Makete 

kwa nyakati tofauti watumishi hao walichukua rushwa kwa mfugaji huyo baada ya kumkuta akilisha  mifugo katika Msitu wa asili wa serikali kitendo ambacho ni kinyume na kifungu cha 15(1)(a) na (2) cha sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa sura ya 329 marejeo ya Mwaka 2024.

Katika mashtaka hayo ambayo yalifunguliwa na taasisi ya kuzuia na kupambana na Rushwa Makete, Mwendesha mashitaka wa TAKUKURU mkoa wa Njombe Daniel Mono ameiomba mahakama hiyo kutoa adhabu kali kwa washitakiwa ili iwe fundisho hasa ukizingatia mkakati wa serikali ni kutunza na kulinda mazingira na maliasili zake

Watuhumiwa hao wamekiri kutenda makosa hayo ya kuomba na kupokea rushwa na ndipo wakahukumiwa na mahakama hiyo, lakini ili kukwepa kifungo cha miaka miwili jela wakalipa faini ya shilingi laki tano kila mmoja.

Washitakiwa Thadeus James Mtui na Florian Gilliad Kilango walichukua rushwa ya kwanza mnamo tar 1/11/2025 kiasi cha Milioni 2 baada ya kukamata mifugo ya Yuda Male na kisha kuchukua rushwa nyingine kiasi cha milioni 6 mnamo 31/1/2026 baada ya kushika tena mifugo ya mfugaji huyo katika Msitu uleule wa asili wa Chimala uliopo kijiji cha Mfumbi kata ya Mfumbi wilayani hapo.

Licha kukiri kosa lao na kisha kulipa faini, Mahakama hiyo imeagiza wawili hao pia kurejesha fedha yote waliyochukua kwa mfugaji huyo kiasi cha shilingi milioni 8 ambaye inaelezwa aliamua kuripoti katika vyombo vya dola kutokana usumbufu alioendelea kuupata ili hali aliwapa rushwa watumishi hao.



Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Serikali kupitia Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora imetangaza mpango wake wa mwaka wa fedha 2026/2027 unaolenga kuimarisha ufanisi, uwazi na utoaji wa huduma bora katika utumishi wa umma.

Akiwasilisha hotuba ya bajeti bungeni Dodoma Aprili 17, 2026,Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete amesema serikali imeweka kipaumbele kikubwa katika ajira, ambapo jumla ya nafasi mpya 45,000 zinatarajiwa kujazwa ili kupunguza upungufu wa watumishi katika taasisi mbalimbali za umma.

Sambamba na hilo, vibali vya ajira mbadala 7,124 vitatolewa kuhakikisha utendaji kazi haukwami pindi watumishi wanapoondoka kazini kwa sababu mbalimbali.

Katika kulinda haki za watumishi, serikali imepanga kuhakiki na kuidhinisha madai ya malimbikizo ya mishahara katika taasisi 425, pamoja na kushughulikia madai ya wastaafu na waliokoma utumishi kutoka kwa waajiri 200. Pia, usimamizi wa malipo ya mishahara utaimarishwa katika taasisi 510 ili kuhakikisha malipo yanafanyika kwa wakati na kwa usahihi.

Kwa upande wa maboresho ya mifumo ya kiutumishi, serikali itafanya uhakiki wa watumishi (staff audit) katika taasisi 127 zinazotumia mfumo wa e-Watumishi, huku taasisi 35 ambazo bado hazijaanza kutumia mfumo huo zitawezeshwa kujiunga nao. Maboresho zaidi yatahusisha kuimarisha teknolojia ya mfumo huo na kuunganisha na mifumo mingine ya serikali pamoja na sekta binafsi.

Aidha, serikali imepanga kuanzisha mfumo maalum wa “dashboard” utakaokusanya na kuwasilisha takwimu sahihi kutoka mifumo mbalimbali ikiwemo e-Watumishi, e-Msawazo, e-Utendaji na Watumishi Portal, hatua inayotarajiwa kuboresha maamuzi ya kiutendaji katika ngazi zote za serikali.

Mpango huo unaonesha dhamira ya serikali ya kuendelea kuboresha utumishi wa umma kwa kuweka mifumo madhubuti, kuongeza ajira na kuhakikisha watumishi wanapata stahiki zao kwa wakati.



Sekta ya Sheria siyo ya huduma ila miundombinu laini kufikia utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050.

Hayo yameelezwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Dkt. Franklin Rwezimula wakati akifungua kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kilichofanyika jijini Dodoma.

Dkt. Rwezimula alisema kuwa Dira ya Taifa 2050 imezingatia na kujikita kwenye Sekta ya Sheria ambapo Sekta ya Sheria ni msingi wa kufikia Dira 2050, mazingira ya sheria yamezingatiwa na kupewa kipaumbele ili kuhakikisha kuwa sheria zinatumika kama miundombinu katika kufanikisha utekelezaji wa Dira hiyo ili kuwaletea wananchi maendeleo.

“Kumekuwa na mtazamo kuwa Sekta ya Sheria inahusika na utoaji wa huduma pekee bali ukweli ni kwamba Sekta hii ni miundombinu muhimu ya kufanikisha utekelezaji wa majukumu na hivyo taifa kujiletea maendeleo,” amesema Dkt. Rwezimula.

Pia, ameipongeza OWMS kwa kuendesha mashauri ya madai na usuluhishi kwa niaba ya Serikali ndani na nje ya nchi kwa ufanisi na weledi na amewakumbusha kuwa lengo la kuwa na Baraza hilo mahali pa kazi ni kuwawezesha wafanyakazi kushauri menejimenti na kushirikiana katika kutekeleza majukumu.

Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi alisema kuwa katika kipindi cha mwezi Julai, 2025 hadi Aprili, 2026 Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali imeendesha jumla ya mashauri 10,400 ya madai ambapo kati ya mashauri hayo, mashauri 642 yalikamilika na OWMS imeshinda mashauri 563 sawa na asilimia 88%.

“Ushindi huu wa uendeshaji wa mashauri kwa niaba ya Serikali na taasisi zake ni dhahiri kuwa OWMS imeitendea haki Serikali,” amesema Dkt. Possi.

Akizungumza kabla ya kumkaribisha Mgeni Rasmi, Naibu Wakili Mkuu wa Serikali, Bi. Alice Mtulo amesema kuwa OWMS inawashirikisha wafanyakazi katika majadiliano ya pamoja ya utekelezaji wa majukumu.

Katika hatua nyingine, Dkt. Rwezimula alizindua Mkakati wa Mawasiliano wa OWMS (OSG Communication Strategy) ambapo Mkakati huo utaiwezesha Ofisi hiyo kuwa na mwongozo wa kufanya mawasiliano ya kimkakati baina ya Ofisi hiyo, wadau na wananchi, kuchambua na kuainisha njia za mawasiliano, ukusanyaji wa mrejesho na namna ya kufanyia kazi ili OWMS iweze kutumia lugha nyepesi na rahisi kuwasiliana na wadau na wananchi kwa ujumla.

Kikao hicho cha Baraza kimeshirikisha wajumbe na wawakilishi wa OWMS kutoka mikoa 18 ya Ofisi hiyo ambapo inatekeleza majukumu yake.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Dkt. Franklin Rwezimula akizungumza na wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali wakati akifungua Mkutano wa Baraza la Ofisi hiyo uliofanyika Jijini Dodoma.
Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi akizungumza na wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali wakati wa Mkutano wa Baraza la Ofisi hiyo uliofanyika Jijini Dodoma.
Naibu Wakili Mkuu wa Serikali, Bi. Alice Mtulo akizungumza na wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali wakati wa Mkutano wa Baraza la Ofisi hiyo uliofanyika Jijini Dodoma.

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Dkt. Franklin Rwezimula (aliyesimama katikati) akiwaongoza wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi la Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kuimba wimbo wa mshikamano daima wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Baraza hilo uliofanyika Jijini Dodoma.



Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Dkt. Franklin Rwezimula (aliyesimama katikati) akikata utepe kuzindua Mkakati wa Mawasiliano wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali (OSG Communication Strategy) baada ya kufungua Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi hiyo uliofanyika Jijini Dodoma. Anayeshuhudia kushoto kwake ni Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Dkt. Franklin Rwezimula (aliyesimama katikati) na viongozi wengine wakionesha Mkakati wa Mawasiliano wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali baada ya kuuzindua wakati wa Mkutano wa Baraza la wafanyakazi wa Ofisi hiyo uliofanyika jijini Dodoma.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Dkt. Franklin Rwezimula (aliyesimama kulia) akipokea zawadi kutoka kwa Wakili Mkuu wa Serikali Dkt. Ally Possi baada ya kufungua Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi hiyo uliofanyika Jijini Dodoma.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Dkt. Franklin Rwezimula akiwa kwenye picha ya pamoja na wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi za mikoa za Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali baada ya kufungua mkutano wa Barza hilo uliofanyika Jijini Dodoma.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Dkt. Franklin Rwezimula (aliyeketi katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali baada ya kufungua mkutano huo uliofanyika Jijini Dodoma.

Na Byera Deus,Bukoba 

Kutokana na Mabadiliko ya bei elekezi ya mafuta iliyoanza kutumika Aprili Mosi mwaka huu  Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) wamekutana na wadau wanaotumia Usafiri wa majini   kufanya   tathmini ya athari za bei ya mafuta na  kujadili uwezekano wa kurekebisha au kuongeza nauli za abiria katika njia mbalimbali za usafiri majini

Afisa Uhusiano wa TASAC Kanda ya Ziwa, Said Mkabakuli, alisema lengo la shirika hilo ni kulinda maslahi ya wananchi pamoja na watoa huduma kwa kuhakikisha kunakuwa na uwiano sawa  katika mabadiliko ya nauli, ili wananchi waweze kuendana na gharama bila kubebeshwa mzigo mkubwa, 

Alisema kuwa  maoni ya wadau wanaotumia vyombo vya majini  kuhusu athari za Ongezeko la bei ya mafuta  yaapaswa kutolewa na kupokelewa bila  kuathiri huku huduma bora zinazotolewa kwa wananchi wanaotoka eneo moja kwenda eneo lingine

"Changamoto mafuta kupanda linapotokea linaathiri pande zote mbili ninachoweza kusema ni kuwa tutoe maoni bila kuegemea upande kwa sababu kama wamiliki vya vyombo vinavyotoa huduma na kusafirisha wateja Vitoe huduma bila kumuumiza sana mwananchi gharama itakayoongezeka isiwe kubwa sana ya kukwamisha huduma"alisema Mkabakuri 

Akizungumza kwa niaba ya Katibu Tawala Mkoa wa Kagera, Katibu Tawala Msaidizi Uchumi na Uzalishaji, Issaya Tendega, alisema Serikali itahakikisha maoni yote yanayokusanywa yanawasilishwa katika mamlaka husika na kufanyiwa kazi kwa wakati, huku akisisitiza kuwa majibu yatarejeshwa kwa wadau kabla ya Aprili 26, 2026 ili kuwezesha maamuzi sahihi.

Alisema kuwa ni vyema mamulaka zikaendelea kufatilia kwa ukaribu ili  bei ya mafuta ikipungua gharama za usafirishaji wa abiria zisiendelee kuwa juu Bali zishuke pia   wananchi wapunguziwe mzigo.

"Tuna huduma nyingi sana zinazoenda visiwani na wananchi wetu wengi na watumishi wanaoishu huko, ni kweli bei ya mafuta Iko juu na athari zimeanza Kujitokeza kama mahitaji ya msingi kupanda ,Hapa inabidi maridhiano kati ya wananchi na wamiliki vya Usafiri majini kwa kuzingatia matakwa halisi ya mamulaka husika ,tunaomba ukaribu huo uendelee siku mafuta ya kushuka basi na wananchi wetu   bei za kwenda visiwani zishuke"alisema Tendega

Kwa upande wa wadau, baadhi yao akiwemo Mwalimu Ivona Bajumuzi, wameipongeza TASAC kwa kuwashirikisha wananchi katika mchakato huo, wakieleza kuwa hatua hiyo inasaidia kuongeza uelewa pale ambapo mabadiliko ya nauli yanapotokea.

Hata hivyo, baadhi ya wadau walioudhuria mkutano huo  wameeleza hofu juu ya ongezeko la nauli kubwa za pambeni ambazo wamiliki wanaweza kujiongezea bila kufuata utaratibu , wakitaka kuwepo kwa suluhisho litakalopunguza gharama  na mamulaka kuweka Ukomo  wa nauli zitakazopangwa bila kuathiri maisha ya watumiaji wa Usafiri wa majini wa Kila siku. 






Singida

Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Singida, kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), imeendesha mafunzo maalum kwa wachimbaji wadogo wa madini yenye lengo la kuongeza uelewa kuhusu uchimbaji salama, wenye tija na unaozingatia utunzaji wa mazingira.

Mafunzo hayo yamelenga kuwajengea wachimbaji uwezo katika matumizi ya teknolojia bora za uchimbaji, usimamizi wa afya na usalama migodini, uongezaji thamani wa madini pamoja na kuimarisha biashara ya madini kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za sekta ya madini.

Akifungua mafunzo hayo yaliyofanyika katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa huo, Mhandisi Sabai Nyansiri, amesema Serikali inaendelea kuweka mazingira rafiki kwa wachimbaji wadogo ili kuhakikisha sekta ya madini inachangia kikamilifu maendeleo ya wananchi na uchumi wa Taifa kwa ujumla.

Ameongeza kuwa mafunzo hayo ni sehemu ya juhudi za Serikali kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo katika kuwawezesha wachimbaji wadogo kuongeza tija, kipato na kuendesha shughuli zao kwa kuzingatia misingi ya usalama, uhifadhi wa mazingira na uendelevu wa rasilimali madini.







(HUMANITARIAN AWARD)

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ametunukiwa tuzo maalum ya  kimataifa ya Ubinadam ya upasuaji wa ubongo, kutokana na mchango wake mkubwa katika kuimarisha sekta ya afya nchini. 

Tuzo hiyo imetolewa leo Aprili 16,2026 na Rais wa Chama cha Madaktari wa Upasuaji wa Ubongo Mgongo na mishipa ya fahamu Tanzania Dkt. Othman W. Kiloloma katika mkutano wa pili  wa kimataifa wa Shirikisho la Jumuiya ya Upasuaji wa ubongo, mgongo na mishipa ya fahamu.

"Kwa niaba ya Chama cha Wataalam wa upasuaji wa ubongo na mgongo tunakutambua na kukushukuru kwa mchango wako mkubwa wa ubinadamu, ni heshima yangu kubwa kukukabidhi tuzo ya ubinadamu ya upasuaji wa ubongo, hongera sana"

Dkt. Kiloloma amesema katika taaluma ya upasuaji wa ubongo, muda ni uhai na mifumo madhubuti ndiyo huamua hatima ya mgonjwa, kupitia uongozi wako thabiti Tanzania imeimarisha uwezo wa kukabiliana na magonjwa hatarishi ya ubongo na uti wa mgongo.

Amesema kuwa, kupitia uwekezaji uliowekwa na Serikali ya awamu ya sita katika huduma za kibingwa na ubingwa bobezi, ujenzi wa rasilimali watu na uimarishaji wa huduma za vipimo, dharura na bima ya afya kwa wote umeokoa maisha na matumaini ya maisha ambayo wengine hawakuwa nayo.

"Tuzo hii haitambui sera pekee, bali utekelezaji na matokeo yameonesha kuwa, uongozi wa kweli unaweka utu wa binadamu katikati ya maendeleo ya taifa" amesema Dkt. Kiloloma


 



Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma
Serikali imeongeza juhudi za kuimarisha zao la pamba nchini kwa kuweka mkazo katika kuongeza tija, kuhakikisha bei yenye uhalisia kwa wakulima, pamoja na kuboresha huduma za ugani na upatikanaji wa pembejeo bora. Hatua hizi zinalenga kuinua ustawi wa wakulima na kukuza mchango wa zao hilo katika uchumi wa taifa.

Akizungumza wakati wa Mkutano wa Wadau wa Tasnia ya Pamba uliofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete jijini Dodoma, Waziri wa Kilimo, Mhe. Daniel Chongolo (Mb), amesema Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wote katika mnyororo wa thamani wa zao la pamba ili kuhakikisha sekta hiyo inakuwa na tija endelevu.

Ameeleza kuwa juhudi hizo zinajumuisha utoaji wa elimu kwa wakulima kuhusu mbinu bora za kilimo, pamoja na kusambaza pembejeo kwa wakati ili kuongeza uzalishaji na ubora wa pamba inayozalishwa nchini.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Pamba, Marco Mtunga, alisisitiza kuwa zao la pamba lina nafasi muhimu katika kukuza uchumi wa viwanda na kuongeza ajira. Alibainisha kuwa Serikali imelenga kuongeza uzalishaji wa pamba kufikia tani milioni 1 ifikapo mwaka 2030.

Aidha, alifafanua kuwa kupitia programu ya BBT–Ugani Pamba, huduma za ugani zimeboreshwa na kusogezwa karibu zaidi na wakulima, hali iliyochangia kuongezeka kwa uzalishaji. Kwa msimu wa kilimo wa 2025/2026, uzalishaji unatarajiwa kufikia tani laki 3, ikiwa ni hatua muhimu kuelekea malengo ya muda mrefu.

Katika mkutano huo, wadau mbalimbali walitoa maoni yao wakisisitiza umuhimu wa Serikali kufanya tathmini za kina za bei ya pamba ili kuhakikisha mkulima anapata faida stahiki. Pia waliomba kuongezwa kwa matumizi ya teknolojia za kisasa za kilimo, pamoja na utoaji wa ruzuku kwa pembejeo muhimu kama vile viuadudu na mbegu bora.

Wakulima nao walieleza mafanikio wanayopata kutokana na kuboreshwa kwa huduma za ugani. Mkulima mmoja kutoka wilayani Chato alieleza kuwa alianza kwa kulima ekari moja na kuvuna kilo 200 za pamba, lakini baada ya kupata elimu na usaidizi wa kitaalamu, sasa anavuna hadi kilo 2,000 katika ekari hiyo hiyo—ongezeko linaloonyesha mchango mkubwa wa huduma za ugani.

Mkutano huo ulihudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Naibu Waziri wa Kilimo, Mhe. David Silinde (Mb); Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Bw. Gerald Mweli; wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo; wakulima; wabunge; wakuu wa mikoa inayolima pamba; wanaushirika; wafanyabiashara; pamoja na wawekezaji.

Kwa ujumla, mkutano huo umeonesha dhamira ya pamoja kati ya Serikali na wadau kuhakikisha zao la pamba linakuwa kichocheo kikubwa cha maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini.










Top News