TUME ya Uchunguzi wa Matukio ya Uvunjifu wa Amani yaliyojitokeza wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, leo Januari 30, 2026, imekutana na Wakili wa kujitegemea Peter Madeleka.

Mkutano huo wa Tume na Madeleka umefanyika katika Ukumbi wa Tanganyika uliopo katika ofisi za Benki Kuu ya Tanzania (BoT) jijini, Dar es Salaam.

Miongoni mwa yaliyojadiliwa ni pamoja na namna matukio hayo yalivyoanza, athari zake kwa watu, mali na miundombinu pia ushauri wa namna ya kuondokana na matukio hayo.

Tume inaendelea kukutana na makundi mbalimbali wakiwemo waathirika wa Matukio hayo.




Na Nasra Ismail, Geita.

Baraza la Madiwani Halmashauri ya Wilaya ya Geita leo Januari 30,2026 limefanya Mikutano wake Maalum kujadili na kupitisha rasimu ya Mpango wa Bajeti kwa mwaka wa fedha 2026/27.

Akiwasilisha rasimu hiyo kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji katika Mkutano Maalum wa Baraza la Madiwani uliofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Halmashauri uliopo Nzera Bi Sarah Yohana ambaye ni Afisa Mipango Halmashauri ya Wilaya ya Geita, ameliomba baraza hilo kupokea mpango wa bajeti ya mwaka 2026/27 yenye jumla ya Shilingi Bilioni 112.8.

Aidha Afisa Mipango Bi Sarah Yohana amelieleza baraza hilo kuwa Bajeti hiyo imezingatia mapendekezo na ushauri uliotolewa na kamati za kudumu za Halmashauri pamoja na Baraza la Wafanyakazi kwa ajili ya kuleta ufanisi katika usimamizi na utekelezaji wa bajeti hiyo.

Bajeti hiyo inajumuisha fedha za mapato ya ndani Kiasi cha Shilingi Bilioni 15.8, Ruzuku ya Mishahara Bilioni 78.9, Ruzuku ya matumizi mengineyo Bilioni 1.5 na Ruzuku ya miradi ya maendeleo Bilioni 16.5

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri Dkt Modest Buchard amelipongeza baraza Hilo kwa namna lilivyoidhinisha mpango huo wa bajeti 2026/2027.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Wilayani Geita Komredi Barnabas Mapande amelieleza Baraza hilo kuwa ili miradi ya maendeleo ikamilike hakuna budi kuweka bidii katika ukusanyaji wa mapato. 

" Ili miradi iende lazima tukusanye mapato kwa kila mmoja kutekeleza wajibu wake kwa kushirikiana Madiwani na wataalam ambao ni watendaji katika Halmashauri" Amesema Komredi Mapande.

Pamoja na hayo, Komredi Mapande ameongeza kuwa ili kufanya kazi vizuri lazima Halmashauri iwe na utulivu na kuwataka Watumishi wa Halmashauri kusimama katika nafasi zao ili kuendana na kasi ya Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Naye Katibu Tawala Wilaya ya Geita Bi Lucy Beda amelipongeza baraza Hilo kwa kuwa na kikao kizuri kwa kupitisha Mpango wa Bajeti 2026/27.

Bi Lucy Beda amesema Halmashauri ya Wilaya ya Geita inavyo vyanzo vingi vya mapato hivyo Halmashauri iendelee kuongeza udhibiti katika ukusanyaji wa mapato ili kufikia adhma ya serikali kufanikisha miradi ya maendeleo.

“Tunalojukumu kubwa la kuongeza usimamizi na ukusanyaji wa mapato” Amesema BI Lucy beda.

Katibu Tawala huyo ameongeza kwa kusema Halmashauri iendelee kufanya kazi kwa umoja na ushirikiano ili kusonga mbele.

Akihitimisha kikao cha Bajeti katika Baraza Hilo, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita Mhe Jumanne Misungwi amesema madiwani na wakuu wa idara wamejipanga kuongeza mapato ya Halmashauri kwa kufata mikakati waliyo azimia.

Mhe Misungwi amewataka Wataalam kuongeza kasi katika ukusanyaji wa mapato na kufanya kazi kwa bidii ili kuisadia Serikali. 

Vilevile Mhe Misungwi ameishukuru Serikali inayo ongozwa na Mhe Dkt Samia Suluhu kwa kazi nzuri anazozifanya na kusema Halmashauri itaendelea kufanya kazi kuendana na kasi yake kuleta maendeleo chanya.










 

Na Mwandishi Wetu- Dar es Salaam.

Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA) leo tarehe 30 Januari, 2026 umepokea ugeni wa wanafunzi 30 wa Kitengo cha Petroleum Engineering kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI), chini ya Chama cha wahandisi wa mafuta (Society of Petroleum Engineers -SPE),waliotembelea Wakala huo kwa lengo la kujifunza kwa vitendo kuhusu utendaji kazi wa PBPA na namna Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (BPS) unavyotekelezwa nchini.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Kaimu Meneja wa Kitengo cha Lojistiki za Mafuta PBPA, Mhandisi Sophia Kidimwa, alisema kuwa wanafunzi hao wamepata fursa ya kuelewa mchakato mzima wa upatikanaji wa mafuta nchini kuanzia hatua za uagizaji hadi usimamizi wa lojistiki za kupokea mafuta.

“Tumepokea ugeni wa wanafunzi wa mwaka wa nne kutoka UDSM na DMI waliokuja kujifunza kuhusu taratibu zote za upatikanaji wa mafuta hapa Tanzania, jinsi mafuta yanavyoingia nchini, mchakato mzima wa uletaji wake pamoja na lojistiki za kupokea mafuta na manufaa ya Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (BPS),” alisema Sophia.

Aliongeza kuwa PBPA imekuwa ikipokea wageni kutoka taasisi mbalimbali zinazopenda kujifunza kuhusu mfumo wa BPS kutokana na mafanikio na manufaa yake kwa Taifa.

“Kama taasisi, tumekuwa tukitoa uelewa huo kwa wageni wetu na wamekuwa wakionyesha kuridhika. Tunaendelea kuwakaribisha wadau wote wanaopenda kujifunza kuhusu Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja,” alisisitiza.

Kwa upande wake, Mhandisi kutoka Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA), Prudence Laurean, alisema wanafunzi hao walipitishwa katika mifumo yote ya PBPA kuanzia hatua za uagizaji wa mafuta hadi mafuta yanapofika kwenye maghala ya kuhifadhia, ikiwemo matumizi ya Mfumo wa SCADA katika ufuatiliaji wa mafuta wakati wa kushushwa kutoka melini kwenda kwenye maghala ya Serikali na binafsi.

“Mafunzo haya ni muhimu sana kwa wanafunzi kwani yanawajengea uelewa wa kina kuhusu kazi za PBPA na faida zitakazowasaidia kitaaluma hapo baadaye,” aliongeza.

Akizungumza kwa niaba ya wanafunzi, Sifrina John, mwanafunzi wa mwaka wa nne Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, alisema ziara hiyo imelenga kuwaunganisha wanafunzi na uhalisia wa kazi katika sekta ya mafuta nchini.

“Lengo letu ni kuunganisha yale tunayojifunza darasani na mazingira halisi ya kazi katika sekta ya mafuta, na kuelewa kwa vitendo jinsi PBPA inavyofanya kazi katika uagizaji na usimamizi wa ugavi wa mafuta nchini,” alisema Sifrina.

Aliongeza kuwa wanafunzi wamefurahishwa na mafunzo waliyoyapata na namna PBPA inavyosimamia ugavi wa mafuta pamoja na mchango wake katika uchumi wa Taifa.

“Tumepata uelewa wa kina kuhusu mchakato wa uagizaji wa mafuta, usimamizi wa ugavi na mchango wa PBPA katika uchumi wa nchi. Mafunzo haya yametujenga kwa kiasi kikubwa kwa kuunganisha nadharia na vitendo,” alisisitiza.

Ziara hiyo ni mwendelezo wa juhudi za PBPA katika kuimarisha ushirikiano na wadau kutoka taasisi mbalimbali nchini sambamba na kukuza uelewa wa vijana kuhusu mifumo ya kimkakati inayosimamia sekta ya mafuta na mchango wake katika uchumi wa Taifa.





Na Seif Mangwangi, Michuzi TV, Arusha.

Msaada wa kisheria wa Samia Legal Aids umeahidi kurudisha tabasamu kwa wananchi kwa kuwapatia msaada wa kisheria katika migogoro inayowakumba hadi pale ufumbuzi unapopatikana.

Akizungumza katika mkutano wa wanasheria kutoka sekretarieti za mikoa wanaotoa msaada wa kisheria kutoka  SAMIA LEGAL AIDS nchi nzima, Mkurugenzi wa sheria ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za mikoa na serikali za mitaa (TAMISEMI) Wakili Richard Odongo amesisitiza kuwa lengo kuu ni  kuhakikisha wananchi wote wanafikiwa kupata huduma za msaada wa kisheria kama inavyoelekezwa.

Aidha  amesema kuwa migogoro itapungua sana iwapo mabaraza ya kata yatatekeleza majukumu yake kwa ufasaha hatua itakayowaondolea mzigo wanasheria wanaotekeleza jukumu hilo.

"Inafahamika kuwa migogoro inayoongoza nchini ni ya ardhi, ndoa na mirathi. Hivyo kwa kikao hiki tumekuja na mkakati wa kutatua migogoro hiyo kwa kuhakikisha kila mkoa tunakuwa na wanansheria wabobezi wawili watakaoshughulikia masauala hayo" amesema Wakili Odongo.

Katika namna hiyo hiyo Mkoa wa mkoa wa Arusha CPA Amos Makalla akimwakilisha Waziri wa Katiba na Sheria amesisitiza uwajibika wa haki katika  kuwasaidia watoto, wanawake na makundi maalum.

Amepongeza mpango wa huduma za kisheria za SAMIA LEGAL AIDS  unaowaokoa maelfu ya wananchi wanyonge kupata haki ya kutatuliwa migogoro yao hususan ya ardhi ambayo ndio kinara.

Kwa upande wake Wakili Tamari Mndeme kutoka ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali nchini, amesema wamegundua kuwa wananchi wote hawafanikiwi kumaliza migogoro yao katika kipindi cha kampeni ya  msaada wa kisheria unapotolewa, hivyo mpango mkakati ni kuwaimarisha wataalam wa sheria waliochaguliwa kusimamia migogoro ya wananchi kila mkoa bila malipo kuwasimamia wananchi mpaka pale watakapofanikiwa.

"Wananchi wengi wanaotafuta msaada wa kisheria uwezo wao kifedha ni mdogo, hivyo SAMIA LEGAL AIDS itawapatia msaada bure bila malipo hadi pale watakapofanikiwa, lengo la Rais wa awamu ya sita wa  jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan ni kuwarudishia wananchi tabasamu" amesema Wakili Tamari.



 



Na Mwandishi Wetu
KAMPUNI ya Airtel Afrika imepata faida baada ya kodi ya Dola za Marekani 586 milioni kwa kipindi cha miezi tisa kilichoisha Desemba 31, 2025, ikiongezeka zaidi ya mara mbili kutoka Dola 248 milioni katika kipindi kilichotangulia, ikichangiwa na faida kubwa za uendeshaji na mapato makubwa kifedha na mabadiliko ya fedha za kigeni.

Katika kipindi hicho, faida ya uendeshaji na mabadiliko ya fedha za kigeni yenye thamani ya Dola 99 milioni ikilinganishwa na hasara ya Dola 153 milioni katika kipindi kilichotangulia, ilichangiwa sana na utendaji wa kifedha wa Airtel Africa.

Ndani ya kipindi cha miezi tisa mapato yalifikia Dola 4,667 milioni, yakiongezeka kwa 24.6% kwa thamani ya sarafu thabiti na 28.3% kwa thamani iliyoripotiwa kutokana na kuimarika kwa sarafu, jambo lililoimarisha misingi ya biashara.

Utekelezaji makini wa mkakati wa Airtel Africa ulipelekea ongezeko la mapato hadi 24.7% katika Robo ya 3, 2026, jambo lililosaidiwa zaidi na kuimarika kwa sarafu, ambapo ongezeko la mapato liliripotiwa kuwa 32.9%.

Katika muhula huo mapato ya huduma za simu yaliongezeka kwa 23.3% kwa sarafu thabiti. Mapato ya data, ambayo ndiyo yanayochangia zaidi kwenye mapato ya kundi, yaliongezeka kwa 36.5% huku mapato ya sauti yakiongezeka kwa 13.5%.

Mapato ya Mobile Money yanaendelea kukua, yakipeleka ongezeko la 29.4% kwa sarafu thabiti. Airtel Money imeendelea kuonyesha ukuaji imara katika mhura huu, ikiipita mafanikio mawaili muhimu.

Idadi ya wateja iliongezeka kwa 17.3% hadi milioni 52.0, huku thamani ya jumla ya malipo yaliyosindikwa kwa mwaka (TPV) kwa Robo ya 3, 2026 ikipita Dola bilioni 210, ikiwa imeongezeka kwa 36%.

Mfumo mpana zaidi na ukuaji wa matumizi ya kidijitali pia ulisababisha ongezeko la 9.8% kwenye ARPU kwa sarafu thabiti.Kutambua fursa kubwa katika masoko yake, Airtel Africa iliweka mkazo wa uwekezaji kulingana na miongozo ya capex iliyorekebishwa iliyotangazwa awali.

Matumizi ya mtaji yalifikia Dola 603 milioni, yakiongezeka kwa 32.2% kutoka kipindi kilichotangulia, na kusaidia upanuzi wa takriban minara 2,500 mipya na upanuzi wa mtandao wa nyuzi za kioo kwa takriban km 4,000, hivyo kufikia jumla ya km 81,500.

Uwekezaji huu umeimarisha upanuaji na uwezo wa mtandao, ukisaidia kuboresha uzoefu wa wateja.

Jumla ya ufikiaji wa idadi ya watu ulifikia 81.7%, ongezeko la alama 0.6% kutoka mwaka uliopita.

Akizungumza kuhusu matokeo hayo, Mkurugenzi Mtendaji wa Airtel Africa, Sunil Taldar, alisema:“Matokeo haya yanaonyesha nguvu ya mkakati wetu, yakionyesha utendaji thabiti wa uendeshaji na kifedha katika biashara zetu zote.”

Katika robo hii, kampuni ilikazia uwekezaji ili kuongeza upanuzi wa mtandao na uwezo wa data huku ikipanua mtandao wake wa nyuzi za kioo. Uwekezaji huu, ukiunganishwa na ushirikiano wa ubunifu, unaleta nguvu zaidi kwa wateja na unatuweka katika nafasi ya kunasa fursa kubwa za ukuaji katika masoko yetu.

Aliongeza kuwa kidijitali, ubunifu wa kiteknolojia, na kuingizwa kwa AI katika uendeshaji vitaimarisha uzoefu wa wateja, kupanua huduma za kidijitali, na kuunganisha vyema huduma za GSM na Airtel Money, hivyo kuwezesha kampuni kukidhi mahitaji yanayoongezeka.

Uchukuzi wa simu mahiri unaendelea kuongezeka, ukiwa na kiwango cha penetration ya 48.1%, huku biashara ya home broadband ikionyesha ukuaji imara, ikionyesha mahitaji yanayoongezeka ya muunganisho wa kasi ya juu na wa kuaminika.

ARPU ya data iliongezeka kwa 16.6% kwa sarafu thabiti na matumizi ya wastani yalifikia GB 8.6 kwa mwezi, ikionyesha athari za kuongeza uwezo wa mtandao. “Juhudi zetu za kuongeza ujumuishaji wa kifedha barani Afrika zinaendelea kupata mwendo mzuri, huku idadi ya wateja wa Mobile Money ikifikia milioni 52, ikipita milestone ya milioni 50,” alisema.

Thamani ya jumla ya malipo yaliyochakatwa (TPV) ya Dola bilioni 210 kwa Robo ya 3, 2026 inaonyesha ukubwa na kina cha wajasiriamali, mawakala, na washirika, ikithibitisha nafasi ya Airtel kama kielelezo muhimu cha ujumuishaji wa kifedha barani Afrika. Kampuni ipo kwenye mstari sahihi kwa ajili kuiorodhesha Airtel Money katika nusu ya kwanza ya 2026.“Mkakati wetu wa kuzingatia wateja unaendesha mwendo mzuri, ukiungwa mkono na uwekezaji wa mtandao, kidijitali, na ushirikiano wa kimkakati,” aliongeza.

Idadi ya wateja jumla iliongezeka kwa 10% hadi milioni 179.4, huku watumiaji wa data wakiongezeka 14.6% hadi milioni 81.8.


FARIDA MANGUBE, MOROGORO 

Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Morogoro kinatarajia kuadhimisha miaka 49 ya kuzaliwa kwa Chama hicho Januari 31, 2026, kwa kufanya shughuli mbalimbali zikiwemo kukagua utekelezaji wa Ilani ya CCM pamoja na kutembelea miradi ya maendeleo katika Wilaya ya Mvomero.

Akizungumza na Michuzi Tv Katibu wa CCM Mkoa wa Morogoro Nuru Ngereja, amesema maadhimisho ya sherehe hizo zitafanyika Turiani Wilani Mvomero na mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Morogoro Mhandisi Joseph Masunga huku kilele  kitafanyika Februari 5 Halmashari ya Mlimba na mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Mwenyekiti wa UVCCM Taifa Ndugu Mohamed Ali Kawaida.

Ngereja amesema kuwa lengo la maadhimisho hayo ni kuhakikisha chama kinajitathmini kwa vitendo utekelezaji wa Ilani yake na kujionea maendeleo yanayotekelezwa kwa manufaa ya wananchi, badala ya kufanya sherehe za kawaida.

Ameeleza kuwa miongoni mwa miradi itakayokaguliwa ni Hospitali ya Wilaya ya Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero, pamoja na miradi mingine ya maendeleo inayotekelezwa ndani ya mkoa huo.

“Maadhimisho haya ni fursa ya chama kujipima, kuona utekelezaji wa Ilani na kusikiliza changamoto za wananchi ili kuzitafutia ufumbuzi,” amesema Ngereja.

Aidha, Katibu huyo wa Mkoa amezungumzia siku 100 za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, akisema kuwa zimeanza kuleta matokeo chanya ndani ya Mkoa wa Morogoro, hususani katika sekta ya afya kupitia utekelezaji wa mpango wa Bima ya Afya kwa Wote.

Amesema mpango huo tayari umeanza kutekelezwa mkoani humo, ukiwa na lengo la kuhakikisha wananchi wanapata huduma za afya bila kikwazo cha gharama.

Ngereja ameongeza kuwa serikali inaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo ndani ya mkoa huo, ikiwemo miradi ya maji, ujenzi na ukarabati wa barabara pamoja na ujenzi wa vituo vya afya, miradi ambayo inalenga kuboresha huduma za kijamii na kuinua maisha ya wananchi.

Amehitimisha kwa kusema CCM Mkoa wa Morogoro itaendelea kushirikiana na serikali katika kuhakikisha miradi hiyo inatekelezwa kwa ufanisi na kwa manufaa ya wananchi.






Na Mwandishi Wetu
MASHABIKI wa soka nchini Tanzania wanatarajiwa kushuhudia mchezo mkubwa wa kimataifa siku ya Jumamosi, tarehe 31 Januari 2026, ambapo klabu ya Young Africans SC (Yanga) itavaana na mabingwa wa kihistoria wa Afrika, Al Ahly ya Misri, katika mchezo wa hatua ya makundi wa Ligi ya Mabingwa Afrika (CAF).

Mchezo huo unatarajiwa kuchezwa katika Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar, kuanzia saa 10:00 jioni, ukiwa ni miongoni mwa michezo inayobeba hadhi kubwa barani Afrika kutokana na historia na ubora wa timu hizo mbili.

Kuelekea mchezo huo, Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya Ulinzi na Usalama limetangaza kuimarisha ulinzi kabla, wakati na baada ya mchezo huo ili kuhakikisha usalama na amani vinaendelea kutawala.

Jeshi la Polisi limetambua kuwa mchezo huo ni wa kimataifa na ni fursa muhimu ya kuitangaza na kujenga heshima ya Taifa, hivyo limeahidi kusimamia kikamilifu hali ya usalama ili kuzuia vitendo vyovyote vya uvunjifu wa amani.

Kupitia taarifa iliyotolewa, Jeshi la Polisi limewahakikishia wananchi, wanachama, mashabiki na wapenzi wa soka kuwa wataendelea kushirikiana nao kuhakikisha mchezo huo unachezwa katika mazingira ya amani na usalama.

Aidha, wananchi na mashabiki wametakiwa kufika uwanjani mapema ili kuepuka msongamano, huku wakikumbushwa kuwa hairuhusiwi kuingia uwanjani na vitu hatarishi ikiwemo silaha au vifaa vinavyoweza kuhatarisha usalama wa watu wengine.

Jeshi la Polisi pia limetoa onyo kali kwa mtu au kikundi chochote kitakachojaribu kutumia mchezo huo kama fursa ya kufanya vitendo vinavyokiuka sheria, likisisitiza kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa kwa yeyote atakayebainika kufanya vitendo hivyo.

Vilevile, madereva wa vyombo vya moto wameonywa kutochukulia mchezo huo kama sababu ya kuvunja au kutotii sheria za usalama barabarani, kwani kutakuwepo na idadi kubwa ya askari wa usalama barabarani watakaosimamia utekelezaji wa sheria, na hatua kali zitachukuliwa dhidi ya watakaokiuka.

Taarifa hiyo imetolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi, ambaye amewataka wananchi wote kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama ili kuhakikisha mchezo huo unakuwa wa kihistoria na wa amani.

📍 Mlimba, Kilombero – Morogoro

Shamba la Chita JKT, lenye ukubwa wa ekari 12,000 zinazolimwa, limepangwa kuwa mfano wa ushirikiano kati ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na Tume ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC). 

Tangu mwaka 2021, Jeshi limekuwa likiendeleza mashamba haya kwa kutumia rasilimali za ndani, likikodisha mitambo na kusawazisha mashamba ili kuongeza tija ya uzalishaji wa mpunga.

Katika ziara yake ya hivi karibuni, Mkurugenzi Mkuu wa NIRC, Bw. Raymond Mndolwa, ametembelea maeneo ya mito yenye miundombinu ya kupeleka maji mashambani na kukutana na uongozi wa JKT katika skimu hiyo na kutoa maagizo mahsusi ya kuimarisha skimu hiyo na kuahidi kuchukua hatua za haraka ndani ya siku 14, lengo likiwa ni kuijengea uwezo CHITA JKT katika uzalishaji wa mazao.

Bw. Mndolwa amesisitiza kuwa upo umuhimu wa kutafuta mbinu ya uhifadhi wa maji, ikiwemo kujenga mabwawa, ili maji mengi yanayopotea yaweze kuhifadhiwa na kutumika kwa Umwagiliaji.Ameeleza

“Kunauhitaji wa kujengwa bwaw jipya, lijengwe kwa kutumia maji kutoka Mto Monyo, ili kusaidia kilimo cha mpunga na shughuli nyingine za matumizi ya maji kwa Chuo cha Jeshi kilichopo eneo hilo” amesema 

Mndolwa ameongeza kuwa Kutokana na changamoto za usawazishaji wa mashamba, usanifu utafanyika upya kwa kushirikisha wataalamu wa Jeshi, NIRC na Mshauri Elekezi

“Ndani ya siku 14, usanifu huo upitiwe ili kuboresha ujenzi unaoendelea na kubaini vyanzo vipya vya kujenga mabwawa” ameongeza Mndolwa 

NIRC ipo tayari kuendelea kushirikiana na Jeshi la kujenga Taifa, kuhakikisha hekari zote 12,000 zinamwagiliwa ipasavyo, na bajeti itatengwa mara usanifu utakapokamilika.

Amesisitiza kuwa maboresho ya vyanzo vya maji na upanuzi wa mashamba katika eneo hilo la JKT ni  sehemu ya mpango wa muda mrefu wa NIRC wa kuongeza tija ya uzalishaji katika kilimo cha Umwagiliaji na kwamba hatua hizo zinalenga kulifanya Shamba la Chita JKT kuwa mfano wa kitaifa wa kilimo cha kisasa, sambamba na malengo ya Dora 2050 na Mpango wa Maendeleo wa Miaka 5 wa serikali.

Naye Afisa Tawala wa Jeshi la Kujenga Taifa, Brigedia Jenerali Hassan Rashid Mabena, alisifu hatua ya NIRC kupitia Mkurugenzi Mkuu Mndolwa, kwa kutembelea na kujionea shughuli zinazofanywa na Jeshi na kuchukua hatua za haraka. 

Amesema ushirikiano huo utaliwezesha Jeshi kufikia malengo yake ya kuongeza uzalishaji wa mazao na kutatua changamoto zinazojitokeza.

Ziara ya Mkurugenzi Mkuu NIRC imeweka mwelekeo mpya wa kimkakati kwa Shamba la Chita JKT, kutoka kilimo kinachotegemea rasilimali za ndani, kuelekea kilimo cha Umwagiliaji chenye mabwawa ya kudumu na mashamba yaliyosawazishwa kitaalamu. 

Ushirikiano wa NIRC na Jeshi unatarajiwa kufanya Chita JKT kuwa nguzo ya uzalishaji wa mpunga na mazao mengine nchini Tanzania na mfano wa ushirikiano wa kitaifa katika sekta ya Umwagiliaji.










 



Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita, amepongeza juhudi za Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA) katika utekelezaji wa mikakati ya kuhamasisha uwekezaji wa ndani, kufuatia ziara ya kikazi ya mamlaka hiyo mkoani Shinyanga ikiwa ni sehemu ya muendelezo wa Kampeni ya Kitaifa ya Uhamasishaji wa Uwekezaji wa Ndani inayoendelea katika mikoa ya Kanda ya Ziwa.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo iliyofanyika Januari 29,2026, Mhe. Mboni alisema kuwa uwepo wa miundombinu bora ni kichocheo muhimu katika kuvutia na kulinda uwekezaji endelevu, akibainisha kuwa Serikali ya Mkoa wa Shinyanga imeendelea kuchukua hatua madhubuti kuboresha mazingira ya uwekezaji ili kuhakikisha wawekezaji wanapata huduma stahiki na mazingira rafiki kwa maendeleo ya biashara na utekelezaji wa miradi ya kimkakati.

Mhe. Mboni alisisitiza kuwa Mkoa wa Shinyanga umejipanga kimkakati kupokea uwekezaji mkubwa zaidi, kupitia maeneo maalum yaliyotengwa rasmi kwa ajili ya uwekezaji, sambamba na kuendelea kuhamasisha uwekezaji wa ndani ili Watanzania wajitokeze kwa wingi kuwekeza katika sekta mbalimbali za kiuchumi ndani ya mkoa huo.

Aliongeza kuwa Ofisi ya Mkoa itaendelea kushirikiana kwa caribou na TISEZA pamoja na wadau wengine wa uwekezaji, kwa lengo la kuharakisha utekelezaji wa miradi, kuondoa changamoto zinazoweza kujitokeza, na kuhakikisha kuwa Shinyanga inanufaika kikamilifu na fursa za uwekezaji zilizopo.

Kwa upande wake, TISEZA iliipongeza Uongozi wa Mkoa wa Shinyanga kwa ushirikiano na utayari wake wa kuweka mazingira wezeshi kwa wawekezaji, huku ikisisitiza kuwa kampeni hiyo inalenga kuwafikia wawekezaji wa ndani, kutoa elimu ya uwekezaji, na kuchochea ushiriki mpana wa Watanzania katika maendeleo ya uchumi wa taifa.









 Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Paul Makonda, amesema Wizara imepatiwa kiasi cha TZS bilioni 2 itakayowawezesha watengenezaji wa maudhui mbalimbali mitandaoni kuimarisha kazi zao na kuwaongezea kipato kupitia majukwaa ya kidijitali.

Amesema hayo Januari 29, 2026 jijini Dodoma na kubainisha kuwa, fedha hizo zimetolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa lengo la kuyawezesha makundi yote ya watengeneza maudhui ikiwemo katika Sekta ya Utalii, Michezo, Habari, Jamii, Muziki, Filamu na sanaa nyinginezo. 

Amebainisha kuwa, zoezi la uandikishaji wa walengwa linaanza rasmi Januari 30 hadi Februari 15, 2026, ambapo watengenezaji wa maudhui wanatakiwa kufika katika ofisi za Halmashauri za Wilaya, Manispaa za Miji na Majiji kupitia vitengo vya habari, ili kuchukua na kujaza fomu za maombi, zikiainisha taarifa binafsi pamoja na shughuli wanazozifanya.

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Dkt. Batilda Buriani, amepongeza uongozi wa Hifadhi ya Taifa ya Saadani kwa kuwa na mazao mengi ya utalii, ikiwemo utalii wa mikutano, unaozivutia taasisi, mashirika na Halmashauri kufanya mikutano yao katika ukumbi uliopo pembezoni mwa fukwe za Bahari ya Hindi ndani ya hifadhi hiyo.

Akizungumza katika Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Mkoa wa Tanga uliofanyika Saadani, amesema uwepo wa vivutio vingi vya utalii ikiwemo wanyamapori, fukwe, utalii wa boti na muingiliano wa maji ya Bahari ya Hindi na Mto Wami, umeifanya hifadhi hiyo kuwa ya kipekee kitaifa.

Dkt. Buriani amesema kutokana na utajiri huo wa vivutio, Mkoa wa Tanga umeandaa mikakati madhubuti ya kuanza kuitangaza Hifadhi ya Taifa ya Saadani kitaifa na kimataifa ili kuongeza idadi ya watalii, mapato na kuifanya Tanga kuwa miongoni mwa mikoa inayoongoza kwa utalii wa asili nchini.

Ameeleza kuwa mkakati huo unaunga mkono juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, za kuitangaza Tanzania kupitia diplomasia ya utalii na kuongeza mchango wa sekta hiyo katika uchumi wa Taifa.

Kwa upande wake, Mkuu wa Hifadhi ya Taifa ya Saadani, Gladys Ng’umbi, amesema hifadhi hiyo ina upekee mkubwa wa kiikolojia unaotokana na muunganiko wa bahari, mito na wanyamapori, hali inayochochea ubunifu wa mazao mengi ya kiutalii.

Amesema mafanikio hayo yameifanya Saadani kukusanya zaidi ya shilingi bilioni 2.5 katika mwaka wa fedha 2024/2025, kutokana na kuongezeka kwa idadi ya watalii wanaotembelea hifadhi hiyo.

Naye Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi kutoka Ofisi ya Kanda ya Mashariki, Fredrick Malisa, amewahamasisha wananchi, taasisi na mashirika kujitokeza kutumia kumbi za mikutano zilizopo ndani ya hifadhi hiyo kujadili masuala ya kiuchumi na maendeleo.

Amesema baada ya kumaliza mikutano yao, washiriki hupata fursa ya kutembelea vivutio vilivyopo ndani ya hifadhi ikiwemo fukwe, wanyamapori na utalii wa boti, hatua inayochochea utalii wa ndani na kuongeza mapato kwa jamii zinazozunguka hifadhi.

Awali, wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Mkoa wa Tanga walipata fursa ya kutembelea vivutio mbalimbali ndani ya Saadani na kueleza kuvutiwa na mazingira na fursa za kiutalii zilizopo.








 


Top News