Na Janeth Raphael - MichuziTv
Serikali imepanga kuwaweka kambini wanafunzi 1,050 waliofanya vizuri zaidi katika Mtihani wa Kidato cha Sita mwaka 2026 na kuchaguliwa kunufaika na mpango wa Samia Scholarship, ambapo watapatiwa mafunzo maalumu ya kuwaandaa kabla ya kuanza masomo yao ya elimu ya juu.
Kambi hiyo itafanyika katika Chuo Kikuu cha Nelson Mandela African Institution of Science and Technology (NM-AIST) jijini Arusha, ambako wanafunzi hao watapata mafunzo mbalimbali yatakayowajengea uwezo wa kitaaluma, uongozi na ubunifu.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma leo, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, amesema mpango huo unatekelezwa kwa maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ukiwa na lengo la kuibua, kukuza na kuendeleza vipaji vya wanafunzi waliofanya vizuri katika masomo ya Sayansi, Teknolojia, Uhandisi na Hisabati (STEM) ili kuzalisha wataalamu watakaochochea maendeleo ya taifa na uchumi wa kisasa.
Profesa Mkenda amesema kati ya wanafunzi hao, 1,000 watapatiwa ufadhili wa kusoma katika vyuo vikuu vya ndani ya nchi, huku wanafunzi 50 bora zaidi wakipewa fursa ya kuendelea na masomo katika vyuo vikuu vya nje ya nchi kwenye fani zinazohitajika katika uchumi wa kidijitali.
Ameeleza kuwa wanafunzi hao wametokana na tahasusi za PCM (Physics, Chemistry and Mathematics), PCB (Physics, Chemistry and Biology), CBG (Chemistry, Biology and Geography), PMG (Physics, Mathematics and Geography), CBA (Chemistry, Biology and Agriculture) pamoja na PMC (Physics, Mathematics and Computer Science).
Kwa mujibu wa Waziri huyo, wanufaika wa ufadhili wa ndani wanapaswa kuomba udahili katika vyuo vikuu vya Tanzania kusomea shahada za Hisabati, Sayansi, Uhandisi au Tiba. Baada ya kupata udahili, watajaza fomu za kujiunga rasmi na mpango wa Samia Scholarship, ambapo Serikali itagharamia asilimia 100 ya ada na gharama za masomo yao.
Aidha, amesema majina ya wanafunzi wote waliochaguliwa yamechapishwa kwenye tovuti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, na kuwataka wahitimu wa Kidato cha Sita kuyakagua pamoja na kufuata taratibu zote zilizowekwa ili kukamilisha mchakato wa kupata ufadhili huo.
Akizungumzia wanafunzi 50 watakaopelekwa kusoma nje ya nchi, Profesa Mkenda amesema wameteuliwa kutoka katika tahasusi za PCM, PMG na PMC, ambazo zinahitaji uwezo mkubwa wa Hisabati ya Juu (Advanced Mathematics).
Amefafanua kuwa uteuzi huo umezingatia alama halisi za mtihani (raw scores) badala ya daraja la ufaulu pekee, akibainisha kuwa wanafunzi wengi wanaweza kupata daraja la "A", lakini wakatofautiana kwa idadi ya alama walizopata.
Profesa Mkenda amesisitiza kuwa Serikali imezingatia uwazi na uadilifu katika mchakato mzima wa uteuzi ili kulinda hadhi ya mpango wa Samia Scholarship.
Amesema mwanafunzi yeyote mwenye mashaka kuhusu kutokuwamo kwenye orodha anaweza kuwasiliana na Wizara ya Elimu kwa ajili ya kupata ufafanuzi wa alama zake kupitia Baraza la Mitihani la Tanzania (NECTA).
Kwa upande mwingine, Waziri huyo amebainisha kuwa asilimia 58 ya wanafunzi waliochaguliwa wanatoka katika shule za serikali, huku asilimia 42 wakitoka katika shule zisizo za serikali, akisisitiza kuwa uteuzi umefanyika kwa kuzingatia vigezo vya ufaulu bila kujali aina ya shule aliyosoma mwanafunzi.