WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, ametimiza ahadi yake ya kutoa pikipiki 10 kwa vikundi vya waendesha bodaboda wilayani Rungwe, mkoani Mbeya, ikiwa ni jitihada za kuwawezesha vijana kiuchumi.

Ahadi hiyo ilitolewa Desemba 18, 2025, wakati Waziri Mkuu alipokuwa akizungumza na wananchi wa Kata ya Kiwira, alipokuwa akitoka wilayani Kyela katika ziara ya kikazi. Katika mkutano huo, Furaha Zuberi Mwakyusa aliwasilisha ombi la kupatiwa pikipiki kwa ajili ya vijana wa bodaboda, ambapo Waziri Mkuu aliridhia na kuahidi kutoa pikipiki 10.

Pikipiki hizo zimekabidhiwa rasmi na Mkuu wa Wilaya ya Rungwe, Jaffar Haniu, kwa niaba ya Waziri Mkuu, katika hafla iliyofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe, Tukuyu.

Katika hafla hiyo, Mkuu wa Wilaya pia alikabidhi pikipiki ya magurudumu matatu (bajaji) kwa Richard Mgongo, Mtendaji wa Kata ya Kiwira mwenye mahitaji maalum, ikiwa ni utekelezaji wa ahadi nyingine ya Waziri Mkuu aliyoitoa siku hiyo hiyo.

Akizungumza wakati wa makabidhiano, Haniu aliwataka waendesha bodaboda kuuenzi ukarimu huo kwa kudumisha amani na mshikamano, sambamba na kaulimbiu ya maadhimisho ya miaka 62 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar inayosisitiza Amani na Mshikamano kwa Maendeleo Endelevu.

Aidha, aliwasisitiza kuzingatia sheria za usalama barabarani na kuzitunza pikipiki walizokabidhiwa ili ziweze kuwa chachu ya maendeleo yao badala ya kuwa chanzo cha ajali au vurugu.

“Tufuate sheria na taratibu zilizowekwa ili pikipiki hizi ziweze kutusaidia,” alisisitiza Haniu.

Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Kamishina Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, Benjamin Kuzaga, alisema Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP), Camillius Wambura, amewaagiza makamanda wa polisi mikoa yote kuhakikisha madereva wa vyombo vya moto wanapatiwa mafunzo ili kupunguza ajali zinazosababishwa na uelewa mdogo.

Naye Richard Mgongo, mnufaika wa bajaji hiyo, aliishukuru Serikali kwa kumuwezesha kupata chombo hicho ambacho kitamsaidia kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi zaidi.

Kwa niaba ya waendesha bodaboda, Furaha Zuberi Mwakyusa alitoa shukrani kwa Ofisi ya Waziri Mkuu kwa ushirikiano uliowezesha kupatikana kwa pikipiki hizo, akisisitiza kuwa wataendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi kuhakikisha wanazingatia sheria na taratibu za usalama barabarani.






Na Farida Mangube Morogoro 

Kemikali inayodaiwa kuwa ni sulphur imemwagika  baada ya gari yenye namba za usajili T196 EMU  mali ya kampuni ya Alhushum  lililokuwa libeba kemikali hiyo kuacha kuacha njia na kugonga miti barabara kuu ya Morogoro–Iringa, karibu kabisa na Bwawa la Mindu.

Michuzi Tv imefika eneo la tukio na kushuhudia jitihada  za dharura zikifanyika kuzuia kemikali hiyo isiingie kwenye bwawa la Mindu iwapo Mvua ikinyesha na kuhatarisha maisha ya wakazi wa Manispaa ya Morogoro ambao asilimia 75 wanategemea maji safi na Salama kutoka kwenye bwawa hilo.

Mamlaka mbalimbali nimefika Katika eneo hilo zikiwemo NEMC, Bonde la Wami-Ruvu, MORUWASA na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji zikiratibu operesheni ya kudhibiti hali hiyo. Hata hivyo, wataalamu kutoka mamlaka hizo wamekataa kuzungumzia tukio hilo kwa kina wakieleza kuwa kipaumbele chao kwa sasa ni kuokoa hali.

Kwa upande wa Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali Kanda ya Kati imesema wataalamu wake wako njiani kutoka Dodoma na watazungumzia tukio hilo baada ya kufika eneo husika.

Hadi majira ya saa Moja na nusu  usiku mwandishi wa michuzi Tv anaondoka Katika eneo la tukio Bado jitihada za kuzuia kemikali hiyo isiingie kwenye mitaro inayotiririsha maji kuelekea bwawani zilikuwa zinaendelea, awali zikihusisha nguvu kazi ya watu kabla ya kuwasili kwa mitambo mizito kusaidia kazi hiyo.








Mkuu wa Mkoa wa Njombe , Mhe. Anthony Mtaka akipokea moja ya mitungi ya gesi uliotolewa na Barrick
Mkuu wa Mkoa wa Njombe , Mhe. Anthony Mtaka akipokea Zawadi ya begi kutoka Afisa Mifumo ya Usalama wa Barrick, Beatrice Amos.

Afisa wa Usalama kutoka Mgodi wa Barrick Mgodi North Mara, Maisori Mniko akizima moto kwa vitendo katika mafunzo ya siku moja ya kupambana na majanga ya moto.

Afisa Msimamizi wa Usalama kutoka Barrick North Mara, Athanas Mtenga akitoa elimu ya usalama mahala pa kazi kwa wajasiriamali wa Mkoani wa Njombe.

Baadhi ya timu ya wafanyakazi wa Barrick kwenye maonesho

Majaji wa OSHA wakipita katika banda la maonesho la Barrick.


*
Elimu ya afya na usalama mahali pa kazi inaendelea kuwafikia wananchi mbalimbali ambao wanatembelea banda la maonesho ya kampuni ya dhahabu ya Barrick kupitia migodi yake ya Bulyanhulu, North Mara na Buzwagi kwenye maonesho ya Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) yanayoendelea mkoani Njombe.

Mbali na elimu hiyo pia wafanyakazi wa Barrick wameshiriki katika programu za kutoa elimu ya afya , usalama na udhibiti wa majanga ya moto kwa makundi mbalimbali mjini Njombe kwenda na kauli mbiu ya mwaka huu isemayo Mazingira bora ya kazi kisaikolojia ni njia ya kuimarisha ustawi wa wafanyakazi na kujenga taasisi imara.

Afisa wa Barrick North Mara , Kitengo cha Dharura na Uokoaji , Maisori Mniko ameeleza kuwa mbali na kutoa elimu kwa wananchi wanaotembelea banda la Barrick mwaka huu wataalamu wa masuala ya usalama wamefikisha elimu ya usalama kwenye makundi mbalimbali nje ya eneo la maonesho ikiwemo mama lishe,madereva wa bodaboda na vikundi vya ujasiriamali vya Wanawake.

Ameongeza kuwa ni muhimu kwa wajasiriamali wa Njombe kujifunza jinsi ya kukabiliana na majanga ya moto.

Amesema mwitikio wa wananchi kupokea mafunzo ya usalama umekuwa ni mkubwa na wengi wao wameuliza maswali mbalimbali kwa wataalamu wa usalama kutoka Barrick ni jinsi gani ya kukabiliana na majanga ya moto na ajali nyinginezo.

Barrick imekuwa ikitekeleza kampeni ya ‘Journey to zero’ ambayo inalenga kuhamasisha afya na usalama kwa wafanyakazi wake ambayo sasa inapelekwa kwa wadau wengine wote kwenye jamii.

“Kampeni yetu ya 'Journey to Zero' inalenga kuhakikisha wafanyakazi wote wa kampuni wanakuwa salama wakati wote wanapokuwa kazini hadi wanaporudi nyumbani hivyo tumehakikisha kampeni hii inavuka mipaka hadi nje ya kampuni kuhakikisha jamii nzima inakuwa salama na ndio maana tunaendelea kuendesha mafunzo ya usalama kwa jamii ili kuhakikisha jamii yote inakuwa salama”, amesema.

Mmoja ya wanufaika wa mafunzo hayo , Mariam Hongoli, kutoka Makambako , amesema kwamba ni muhimu kwa wakazi wa Njombe na vitongoji vyake kujifunza mambo ya kukabiliana na ajali kama vile za moto kwa maslahi mapana ya familia na jamii kwa ujumla.

“Mafunzo haya ni muhimu kwa sababu hata ukiwa nyumbani na watoto unaweza kukabiliana na majanga kama ya moto kwa ufanisi na kuuzima baada ya kupata elimu hii,” amesema Hongoli.

Wakati huo huo banda la maonesho la Barrick limekuwa likitembelewa na viongozi mbalimbali na Serikali na wananchi ambao wameweza kuona vifaa mbalimbali vya kisasa vya usalama na udhibiti wa majanga mbalimbali ikiwemo moto pia kupata mafunzo kutoka kwa wataalamu mbalimbali wa usalama.

Mkuu wa wilaya ya Njombe Juma Sweda ni miongoni mwa wageni waliotembelea banda la Barrick katika maonesho hayo na kupongeza kampuni kwa kuwekeza katika vifaa vya usalama vya teknolojia ya kisasa sambamba na kuwa na programu za kutoa elimu ya Afya na Usalama Mahali pa Kazi kwenye jamii nje ya migodi yake.

Usalama ni sehemu muhimu ya DNA ya Barrick. Katika kudhihirisha hilo migodi yake nchini imekuwa ikishinda tuzo mbalimbali zinazotolewa na taasisi za nchini na za nje.

Mkuu wa Mkoa wa Njombe , Mhe. Anthony Mtaka akipokea zawadi ya begi kutoka Afisa Mifumo ya Usalama wa Barrick, Beatrice Amos.

Mkuu wa Wilaya ya Wanging’ombe akipokea moja ya mtungi wa gesi ulitolewa na Barrick kwa ajili ya kusaidia wajasiriamali.


Afisa Usalama wa Barrick North Mara , Maisori Mniko akitoa mafunzo jinsi ya kuzima moto kwenye mafunzo yaliyoendeshwa na Mgodi wa Barrick North Mara









Wajasiriamali kutoka Mkoa wa Njombe na vitongoji vyake wakiwa kwenye picha ya pamoja na wakufunzi na maafisa usalama kutoka Migodi wa Barrick.

Na.Ashura Mohamed -Arusha

Taasisi kongwe ya dini ya kiislamu ya Twariqa Tulqadirya Arazakia Jailania Tanzania yenye makao yake makuu mkoani Arusha, imedhamiria kufanya sensa ya watu  na mali za taasisi hiyo ili kupata Idadi sahihi ya waumini wake.

Lengo la  zoezi hilo ni kuweza kufanya kazi kwa Ufanisi na kuyafahamu makundi  mbali mbali yaliyomo katika taasisi hiyo yakiwemo  makundi ya Viongozi Vijana,Wanawake,Walemavu,Yatima,Wajane na Wagane ili waweze kupatiwa huduma stahiki katika Mikoa yote ya Tanzania .

Akizungumza na Vyombo vya Habari mkoani Arusha Mwenyekiti wa Twariqa Taifa Shekhe  Mubaraka Salim Gahran amesema kuwa taasisi hiyo  ilifanya sensa ya kitwariqa  mnamo mwaka 1932,ambapo imepita kipindi kirefu bila zoezi hilo kufanyika hali ambayo inapelekea tasisi kushindwa kuwa na Idadi kamili ya watu  pamoja na mali zilizopo sasa.

Shekhe  Gahrani amesema kuwa  pia Ofisi yake imeona  ni vema kufanya uhakiki wa mali zilizopp kwa kuwa tangu kiongozi wao  Daruweshi Mti Mkavu alipofariki takribani mwaka mmoja na nusu  kuna baadhi ya vitu wanapaswa kuviweka sawa ili kuhakiki mali zote na kuepusha migogoro isiyo ya lazima ndani yao ikiwa ni pamoja na watu binafsi kujimilikisha mali za taasisi hiyo nchini.

"Hii ni sensa ya kawaida ya kitwariqa na inawahusu wanatwariqa wa Daraweshi Mti Mkavu na tunataka kuhakiki  kila kitu kuanzia Idadi ya Waridi wetu waliopata Ijaza,Elimu zao za kawaida,kufahamu haya yote itatuwezesha sisi  Viongozi kujua mahitaji yao na tuna watu wa aina gani na tunawahudumiaje na kwa namna gani bila kusahau migogoro isiyo ya lazima  na isielewele vinginevyo.Alisisitiza Shekhe Gahran 

Nae katibu mkuu wa twariqa Taifa shekhe  Haruna Hussein Lotha ameiomba serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kuwapa Ushirikiano wakati wa zoezi hilo ili kufanya zoezi hilo kutekelezwa kwa utulivu na kwa kufuata taratibu.

Shekhe Haruna Hussein amesema kuwa tangu wameingia madarakani hawajui idadi ya waumini wao,majengo wala mali walizonazo ili kuwasaidia kujua mapungufu yaliyopo na kisha kuboresha kwa kuwa kazi ya dini ni kujenga Imani za watu na kuwahudumia kiroho.

"Taasisi  yetu imekuwa ikishirikiana  na serikali yetu kila eneo hivyo tunatazamia kuwa mashirikiano haya  yatakuwa endelevu na  pia tumetumia vyombo vya habari ni kuhakikisha jamii inaendelea  kupata taarifa kwa wakati na zoezi litakapoanza katika mikoa yote ya Tanzania,liwe rahisi "Amesisitiza Katibu Lotha.

Pichani ni Viongozi wa Makundi Mbali mbali wa Taasisi ya TWARIQA TULQADIRIYA JAILANIA TANZANIA wakiongizwa na Mwenyekiti wake Taifa Shekhe Mubarak Salim Gahran na Katibu Mkuu Taifa Sheikh Haruna Hussein  mara baada ya kumaliza kikao Cha ndani.
Mwenyekiti wa TWARIQA Taifa Shekhe Mubarak Salim Gahran wa Pili kulia akiwa na Viongozi Wengine wakati wakizungumza na Vyombo vya Habari


Na Mwandishi Wetu

Tasnia ya filamu nchini imepata pigo kufuatia kifo cha msanii mkongwe, Mzee Kambi, kilichotokea leo Aprili 27, 2026.

Taarifa za kifo hicho zimethibitishwa na Msemaji wa Shirikisho la Filamu Tanzania, Coletha Raymond, aliyesema kuwa msanii huyo alifariki dunia ghafla alipokuwa akiendelea na shughuli zake za kazi.

Akizungumza kuhusu tukio hilo, Coletha alisema Mzee Kambi alikuwa ametoka mkoani Tabora kikazi na aliporejea alielekea moja kwa moja katika shughuli zake kwenye studio za Pilipili, kabla ya kuanza kujisikia vibaya.

“Ni kweli tumempoteza Mzee Kambi. Alikuwa ametoka Tabora na alipofika alienda moja kwa moja kazini katika studio za Pilipilibl. Akiwa kazini ndipo alipozidiwa ghafla na kukimbizwa hospitali, lakini kwa bahati mbaya alifariki dunia,” alisema Coletha.

Aliongeza kuwa chanzo cha kifo kinahusishwa na matatizo ya kiafya yaliyokuwa yakimsumbua, ikiwemo presha na kisukari.

Aidha, alisema Shirikisho la Filamu Tanzania linaendelea na taratibu za ndani kwa kushirikiana na familia ya marehemu ili kupanga mipango ya mazishi, ambapo taarifa zaidi zitatolewa baadaye.

Kifo cha Mzee Kambi kimeacha pengo kubwa katika tasnia ya filamu nchini, ambapo amekuwa mmoja wa wasanii waliotoa mchango mkubwa katika kukuza sanaa hiyo kwa muda mrefu. 
Na MWANDISHI WETU,

Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) umeendelea kuimarika kwa kasi, ukifikia thamani ya shilingi trilioni 11.2 hadi Machi 2026 kutoka trilioni 4.3 mwaka 2020, hatua inayoakisi ukuaji wa uwekezaji, uimara wa usimamizi na kuongezeka kwa ushiriki wa wananchi kupitia Hifadhi Skimu.

Ukuaji huo umeambatana na upanuzi wa huduma za hifadhi ya jamii, hususan kupitia hifadhi skimu zinazolenga kuwafikia wananchi waliojiajiri, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuongeza wigo wa wanachama na kuimarisha ushirikishwaji wa makundi mbalimbali ya jamii katika mfumo wa hifadhi ya jamii.

Akizungumza jijini Dodoma tarehe 27 Aprili 2026 wakati akifungua Mkutano wa 56 wa Baraza Kuu la Wafanyakazi wa NSSF, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Mhe. Deus Sangu, alisema mafanikio ya Mfuko yanatokana na mageuzi ya usimamizi, uwekezaji wenye tija na matumizi ya teknolojia katika utoaji wa huduma.

Alisisitiza kuwa hifadhi skimu ni nguzo muhimu ya mustakabali wa hifadhi ya jamii nchini, akibainisha kuwa Serikali inalenga kuhakikisha Watanzania wengi zaidi, hususan waliojiajiri, wanajumuishwa katika mfumo huo.

“Upanuzi wa hifadhi skimu ni hatua muhimu ya kuhakikisha hakuna Mtanzania anayebaki nje ya mfumo wa hifadhi ya jamii,” alisema Mhe. Sangu.

Waziri huyo pia aliipongeza NSSF kwa mchango wake katika uchumi wa taifa kupitia uwekezaji katika miradi mbalimbali ya maendeleo inayozalisha ajira na kuchochea ukuaji wa sekta binafsi, akitaja kiwanda cha sukari cha Mkulazi kuwa mfano wa uwekezaji wenye tija.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Bw. Masha Mshomba, alisema mafanikio hayo yametokana na usimamizi madhubuti wa fedha, uwekezaji salama na matumizi ya mifumo ya TEHAMA iliyofikia takribani asilimia 99 ya huduma.

Alisema katika Mpango Mkakati wa miaka mitano (2026/27–2030/31), NSSF inalenga kufikia thamani ya shilingi trilioni 24.7 ifikapo Juni 2031, pamoja na kuongeza wanachama hadi milioni 6.6, huku mkazo ukiwekwa katika kuimarisha mpango wa Hifadhi Skimu na kuzingatia misingi ya mazingira, jamii na utawala bora (ESG). Katika kupata hati safi za ukaguzi kutoka Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), mafanikio hayo yametokana pia na Mfuko kufuata misingi ya utawala bora, uwazi, uwajibikaji na uwekezaji wenye tija, hali inayoendelea kuimarisha imani ya wadau na umma kwa ujumla.

Pamoja na mafanikio hayo, Mfuko unaendelea kukabiliana na changamoto mbalimbali ikiwemo baadhi ya waajiri kutowasilisha michango kwa wakati, kuwasilisha michango chini ya kiwango halisi, pamoja na uelewa mdogo wa masuala ya hifadhi ya jamii kwa baadhi ya makundi ya wananchi, hali inayopatiwa ufumbuzi kupitia elimu na uhamasishaji unaoendelea.

Katika hatua nyingine, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF ametoa pongezi kwa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, akibainisha kuwa Serikali ya Awamu ya Sita imeweka mazingira bora na wezeshi ya ufanyaji kazi, uwekezaji pamoja na biashara, jambo lililochochea ongezeko la wanachama na uimara wa mifumo ya hifadhi ya jamii.

Katika hatua nyingine, Waziri Sangu alieleza kuwa mipango ya Mfuko inaendana kikamilifu na mipango mikuu ya Serikali ikiwemo Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 na Sera ya Taifa ya Kinga ya Jamii. Alisema Serikali inalenga kuhakikisha ifikapo mwaka 2050, takribani asilimia 70 ya Watanzania watakuwa wamefikiwa na mifumo ya hifadhi ya jamii kupitia upanuzi wa Hifadhi Skimu na mifumo jumuishi ya kinga ya kijamii.

Waziri huyo alisema mafanikio ya sekta hiyo ni sehemu ya mwelekeo mpana wa taifa wa kujenga uchumi shirikishi unaomlinda kila Mtanzania.

Mkutano huo wa 56 wa Baraza Kuu la Wafanyakazi wa NSSF unajadili Mpango Mkakati wa Nane pamoja na bajeti ya mwaka wa fedha 2026/27, likiwa ni jukwaa muhimu la kuweka mwelekeo wa baadaye wa Mfuko na mustakabali wa hifadhi ya jamii nchini.


















Na Mwandishi Wetu,Michuzi TV.

MKURUGENZI Mtendaji wa Taasisi ya UONGOZI Kadari Singo amesema kwamba madini ni muhimu si tu kwa rasilimali za kiuchumi bali pia ni nyenzo ya kuleta mabadiliko ya kweli katika maendeleo ya Afrika. 

Hivyo ametoa mwito kwa nchi za Afrika kushirikiana, kuweka sera madhubuti, na kuwekeza katika sekta ya madini ili kuhakikisha manufaa yake yanawafikia wananchi wote.

Singo ameyasema hayo leo  Aprili 27, 2026, jijini Addis Ababa nchini Ethiopia wakati wa mkutano wa Jukwaa la Kikanda lililoandaliwa na Tume ya Uchumi ya Umoja wa Mataifa kwa Afrika kwa kushirikiana na Taasisi ya UONGOZI.

Kauli mbiu katika jukwaa hilo inasema  “Kuchangamkia Madini Muhimu ya Afrika kwa Ajili ya Ujenzi wa Viwanda Kijani na Maendeleo Endelevu.” 

Singo katika hutuba yake iliyoangazia nafasi ya Afrika katika mustakabali wa uchumi wa dunia unaozingatia nishati safi, amesisitiza nchi za Afrika zinapaswa kushirikiana, kuweka sera madhubuti na kuwekeza katika sekta ya madini ili manufaa yake yanawafikia wananchi wote

“Jukwaa hili limeweka msingi muhimu wa mijadala itakayochochea hatua za vitendo, huku likisisitiza kuwa mustakabali wa Afrika uko mikononi mwa Waafrika wenyewe, kupitia uongozi bora, ushirikiano, na matumizi sahihi ya rasilimali zake.”

Pia umuhimu wa kuwekeza katika uchakataji wa madini ndani ya nchi, ili kuongeza thamani, kuunda ajira, na kukuza uchumi wa viwanda huku akieleza tafiti zinaonyesha uwekezaji katika sekta hiyo unaweza kuongeza hadi dola bilioni 24 katika pato la taifa kwa mwaka na kuunda zaidi ya ajira milioni 2.3.

“Afrika inaongozwa na sera kama Africa Mining Vision na African Green Minerals Strategy, ambazo zinalenga kuimarisha viwanda, kuongeza thamani ya madini, na kuhakikisha maendeleo jumuishi. Pia, juhudi za kuanzisha minyororo ya thamani ya kikanda, kama ule wa betri na magari ya umeme unaoanzia Kongo na Zambia, zinaonyesha dhamira ya bara kujenga uchumi shindani.”

Amesema kupitia  mikakati ya pamoja na mifumo kama Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA), bara linaweza kubadilisha utajiri wake wa madini kuwa chanzo cha ustawi endelevu huku akisema Afrika inakadiriwa kumiliki karibu asilimia 30 ya hifadhi ya madini muhimu duniani.

Baadhi ya madini hayo cobalt, lithium, graphite na madini adimu (rare earth elements). Kwa mfano, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo huzalisha zaidi ya asilimia 70 ya cobalt duniani, huku nchi kama Zimbabwe, Mali, Tanzania na Msumbiji zikiwa na akiba kubwa ya lithium na graphite.

“Mahitaji ya madini haya yanatarajiwa kuongezeka kwa kasi ifikapo mwaka 2050, hasa kutokana na mabadiliko ya dunia kuelekea nishati safi. Hii inaipa Afrika fursa ya kipekee ya kukuza uchumi wake kupitia viwanda na kuongeza thamani ya rasilimali zake.”

Kuhusu changamoto ya uongezaji thamani amesema licha ya utajiri huo, sehemu kubwa ya madini ya Afrika husafirishwa nje yakiwa ghafi, hali inayopunguza manufaa ya kiuchumi kwa nchi husika. Inakadiriwa kuwa ni takribani asilimia 2 tu ya biashara ya madini hufanyika ndani ya bara la Afrika.

Wakati huo huo Waziri Mkuu wa zamani wa Ethiopia, Hailemariam Dessalegn, ameonya kuwa Afrika iko katika hatari ya kubaki maskini ikiwa itaendelea kuuza nje madini ghafi badala ya kuendeleza viwanda vya kuyachakata ndani ya nchi.

Amesisitiza bara hilo linaweza kukosa kunufaika na uchumi unaokua kwa kasi wa nishati safi licha ya utajiri wake mkubwa wa madini.Afrika ina akiba kubwa ya rasilimali muhimu kama vile cobalt, lithium, shaba na manganizi—madini muhimu kwa magari ya umeme, betri na mifumo ya nishati jadidifu.

Hata hivyo, madini mengi husafirishwa nje yakiwa ghafi, jambo linalopunguza ajira, ujuzi na ukuaji wa viwanda. Dessalegn alionya kuwa mpito wa nishati duniani unaweza kurudia mifumo ya kihistoria ambapo Afrika husambaza malighafi huku utajiri ukizalishwa kwingineko.







Na Mwandishi Wetu.

Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) imepokea ujumbe wa ngazi ya juu kutoka Serikali ya Shirikisho la Somalia kwa ajili ya mafunzo ya kujenga uwezo katika utumishi wa umma, hatua inayoonesha kuimarika kwa ushirikiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.

Mafunzo hayo yanafanyika katika Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) jijini Dar es Salaam, yakihusisha watumishi kutoka Idara ya Masuala ya Baraza la Mawaziri chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu wa Somalia. Lengo kuu ni kuimarisha mifumo ya uratibu wa serikali, usimamizi wa kumbukumbu, ulinganifu wa sera na ufuatiliaji wa maamuzi.

Hafla ya ufunguzi ilihudhuriwa na viongozi waandamizi wa serikali, akiwemo Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Xavier Daudi Mrope, aliyemwakilisha Serikali ya Tanzania.

Katika hotuba ya ufunguzi, Mkuu wa Chuo na Afisa Mtendaji Mkuu wa TPSC, Dr. Ernest Mabonesho alieleza kuwa mpango huo ni hatua muhimu katika kuimarisha taasisi za umma na kuongeza ufanisi wa utendaji wa serikali. Chuo hicho, kilichoanzishwa rasmi mwaka 2000 baada ya kuunganishwa kwa taasisi za mafunzo ya utumishi wa umma, kimeendelea kuwa kitovu cha ubora katika mafunzo, utafiti na ushauri wa kiutawala.

Imeelezwa kuwa mpango huo umeandaliwa kwa ombi la Serikali ya Somalia, kufuatia majadiliano kati ya TPSC na Ofisi ya Waziri Mkuu wa nchi hiyo. Mafunzo yanajumuisha nadharia, vitendo na uzoefu wa taasisi mbalimbali, yakilenga kuwapatia washiriki mbinu zitakazoweza kutumika katika kuboresha mifumo ya utawala nchini Somalia.

Mpango huo pia umeelezwa kuwa ni matokeo ya kuimarika kwa uhusiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Somalia, hasa baada ya ziara ya ngazi ya juu ya Serikali ya Tanzania nchini Somalia mwezi Desemba 2025, iliyoweka msingi wa ushirikiano katika maendeleo ya sekta ya umma.

Washiriki na viongozi wamebainisha kuwa mbali na kujenga ujuzi, mafunzo hayo yanatarajiwa kuimarisha mitandao ya kitaaluma na ushirikiano wa muda mrefu kati ya nchi hizo mbili.

Hatua hii inaonesha nafasi ya Tanzania katika kusaidia maendeleo ya taasisi za umma katika ukanda huu, huku nchi mbalimbali zikiongeza juhudi za kushirikiana kuboresha utawala na utoaji wa huduma kwa wananchi.

Mkuu wa Chuo na Afisa Mtendaji Mkuu wa TPSC, Dr. Ernest Mabonesho  akizungumza wakati wa   mafunzo ya kujenga uwezo watumishi wa Serikali ya Somalia  leo jijini Dar es Saam.
Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Xavier Daudi Mrope akiwa kwenye za pamoja
Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Xavier Daudi Mrope akizungmza wakati wa kufungua  mafunzo ya kujenga uwezo  kwa watumishi wa Serikali ya Somalia Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), jijini Dar es Salaam
Sehemu ya washiriki wa Mafunzo hayo.

Top News