WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Januari 31, 2026 amewasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) ambapo anatarajiwa kumwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika hafla ya Utoaji wa Tuzo za kitaifa za Uhifadhi na Utalii (The Serengeti Awards).

Pia, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu atatembelea Hifadhi ya Taifa ya Arusha ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Mhe. Rais Dkt. Samia katika kukuza Utalii nchini.







▪️Lengo ni kurahisisha upatikanaji wa mitaji na mikopo

▪️Mama Lishe Mtumba kugaiwa mashamba kulima mbogamboga

▪️Majiko 1000 yatolewa kwa Mama Lishe

▪️Mtumba wamuunga mkono Rais Samia juu ya matumizi ya Nishati safi


Mbunge wa Jimbo la Mtumba, Mh. Anthony Mavunde kwa kushirikiana na Kampuni ya Oryx leo amekabidhi jumla ya majiko 1,000 ya gesi kwa mama lishe na baba lishe wa Jimbo la Mtumba, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuunga mkono jitahada za Mh. Rais Dkt. Samia S. Hassan  katika kukuza matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano hayo, Mavunde amesema mpango huo unalenga kuboresha afya za mama na baba lishe, kuongeza ufanisi katika shughuli zao za kila siku pamoja na kulinda mazingira kwa kupunguza matumizi ya mkaa na kuni.

Amesema kuwa Wananchi wa Mtumba kwa kushirikiana  Serikali wataendelea kuweka mazingira rafiki kwa wajasiriamali wadogo ikiwemo upatikanaji wa nishati safi kwa makundi mbalimbali ya jamii ili kupunguza matumizi ya kuni na mkaa.

Mavunde pia ameahidi kuanzisha klabu za mama lishe katika kila kata za Jimbo la Mtumba zitakazosaidia kuwaunganisha mama lishe na kuwapatia elimu ya ujasiriamali, uanzishwaji wa miradi ikiwemo mashamb ya kilimo cha Mboga mboga, usimamizi wa fedha pamoja na kuwawezesha kupata mikopo kwa urahisi ili waondokane na mikopo kandamizi maarufu kama kausha damu.

Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Mafunzo kutoka kampuni ya Oryx Gas, Peter Ndomba, amewataka mama lishe na baba lishe kuacha kabisa matumizi ya mkaa na kuni akisema nishati hizo zimekuwa zikisababisha madhara makubwa ya kiafya ikiwemo magonjwa ya mfumo wa hewa, macho na moyo kutokana na moshi unaotokana na matumizi yake.

Kwa upande wao, mama lishe na baba lishe waliopokea majiko hayo wameishukuru Mh. Mavunde kwa msaada huo wakisema utawapunguzia adha ya kuni na mkaa, kuboresha mazingira ya kazi na kuongeza ufanisi katika shughuli zao za kila siku. 









Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Alhaj Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amewataka Waumini wa Dini ya Kiislamu kujipamba na Qurani Tukufu, kuishi kwa kufuata miongozo na mafundisho yake pamoja na kuifanya Qurani kuwa dira ya maisha yao ya kila siku.

Alhaj Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo tarehe 31 Januari 2026 aliposhiriki Mashindano ya Kimataifa ya Kuhifadhi Qurani, yaliyoandaliwa kwa ushirikiano wa Taasisi ya Altijarah Al Arabia ya Oman na Afisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar, yaliyofanyika katika Msikiti wa Jamiu Zanzibar, Kiembe Samaki, Mkoa wa Mjini Magharibi.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amewanasihi Waumini wa Dini ya Kiislamu pamoja na Wananchi kwa ujumla kushikamana, kuishi kwa umoja, kusaidiana na kudumisha maadili mema ili kupata baraka za Mwenyezi Mungu.

Halikadhalika, amesisitiza umuhimu wa kuishi kwa kupendana, kuimarisha malezi bora ya vijana pamoja na kulinda amani na utulivu wa nchi, akieleza kuwa misingi hiyo ni nguzo muhimu ya maendeleo ya jamii na Taifa kwa ujumla.

Rais Dkt. Mwinyi ameipongeza Taasisi ya Altijarah Al Arabia ya Oman pamoja na Afisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar kwa kufanikisha mashindano hayo, pamoja na mchango wao mkubwa katika kuihudumia jamii kupitia sekta za elimu, afya, chakula na huduma za kijamii kupitia kambi mbalimbali. Amesisitiza umuhimu wa kuendeleza na kuimarisha ushirikiano kati ya Taasisi hizo na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Vilevile, Rais Dkt. Mwinyi amewapongeza washiriki wa mashindano hayo na kuwahimiza kuendelea kushikamana na Qurani Tukufu sambamba na taaluma walizonazo ili kufanikisha mafanikio zaidi duniani na Akhera.

Mashindano hayo ya Kimataifa yamehusisha washiriki sita kutoka nchi za Ujerumani, Uganda, Tanzania, Urusi, Canada na Brazil, ambapo mshiriki Ndg. Usama Barghouth kutoka Ujerumani ameibuka mshindi wa kwanza na kutunukiwa kombe, cheti pamoja na zawadi ya shilingi milioni 20.












Na Mwandishi wetu Dodoma.

Bodi ya Wataalamu wa Ununuzi na Ugavi (PSPTB) iliyoanzishwa mwaka 2007 kwa Sheria ya Bunge Namba 23 ikiwa na Jukumu la kusimamia Taaluma na Wataalam wa ununuzi na Ugavi wa Serikali na Sekta Binafsi

Bodi hiyo huendesha mitihani ya kitaaluma kwa wataalam wa ununuzi na Ugavi katika nafasi tofauti

Bodi hiyo imetangaza rasmi matokeo ya mitihani ya 32 ya PSPTB iliyofanyika Tarehe 01-05 Desemba 2025

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dodoma Mkurugenzi Mtendaji wa PSPTB Godfred Mbanyi amesema jumla ya watahiniwa wapatao 1,291 walisajiliwa ili kufanya mitihani hiyo ambapo watahiniwa 1,223 walifanya mitihani hiyo huku Watahiniwa 68 walikosa mitihani husika kwa sababu mbali mbali.

Mbanyi amesema watahiniwa 595 sawa na asilimia 48.7 wamefaulu kati ya Watahiniwa hao 1,223 na watahiniwa 589 sawa na asilimia 48.2 watarudia masomo yao, na Watahiniwa 39 sawa na asilimia 3.2 wamefeli na wataanza upya masomo yao katika ngazi husika.

Aidha Mbanyi amesema Jumla ya Watahiniwa wawili (2) wa ngazi ya CPSP walikamatwa wakijihusisha na vitendo vya ukiukwaji wa taratibu za mitihani kwa kuingia ndani ya vyumba vya mitihani wakiwa na karatasi ambazo inasadikika walikusudia kuzitumia kuwasadi kujibu mitihani hiyo.

Bodi ya Wakurugenzi imeielekeza kamati ya usaili na nidhamu kushughulikia suala hilo na wahusika wakikutwa na hatia basi itoe adhabu kali kwa mujibu wa kanuni zilizopo, na matoke ya Watahiniwa hao yamezuiliwa na wahusika wataitwa mbele ya kamati husika ikiwa ni sehemu ya kuwapa haki ya kusikiliza.

Mbanyi ametoa wito kwa Watahiniwa wa mitihani ya PSPTB, wanafunzi wa vyuo na kwa wazazi na watahiniwa waliokosa alama za kutosha kuwafanya wafaulu mitihani hiyo wanahimizwa kujisajili tena na kurudia masomo yao kwenye mitihani iliyopangwa kufanyika mei 2026.

Hata hivyo mbanyi amewataka Watahiniwa wote wa fani ya ununuzi wa Ugavi wajiepushe na vitendo vya ukiukwaji wa kanuni na taratibu za mitihani kwani PSPTB haitasita kuwachukulia hatua kali ili kuhakikisha maadili katika tasnia ya Ununuzi na Ugavi inaenziwa na wadau wote.





Na Mwandishi Wetu, Manyara

Zaidi ya kaya 2,000 zenye uhitaji maalum mkoani Manyara zinatarajiwa kunufaika na msaada wa vyakula unaotolewa na Mati Foundation, ikiwa ni sehemu ya mpango wa kampuni ya Mati Super Brands Ltd wa kurejesha sehemu ya faida yake kwa jamii inayozunguka maeneo ya uzalishaji na biashara zake.

Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada wa awamu ya kwanza kwa kaya 37 katika Kata ya Bagara, Wilaya ya Babati, Meneja wa Mradi wa Mati Foundation, Isack Piganio, amesema mpango huo unalenga kusaidia makundi yaliyo katika mazingira magumu, yakiwemo kaya zenye mahitaji maalum, ili kupunguza changamoto za maisha wanazokabiliana nazo kila siku.

Piganio ameeleza kuwa msaada huo wa vyakula ni sehemu ya dhamira ya taasisi hiyo kushiriki kikamilifu katika juhudi za kijamii kwa kushirikiana na Serikali na wadau wengine wa maendeleo, huku akisisitiza kuwa lengo la sasa ni kuongeza wigo wa msaada huo ili kuwafikia walengwa wengi zaidi.

“Lengo letu ni kuhakikisha kaya nyingi zaidi zenye uhitaji zinanufaika. Tunatarajia kufikia takriban kaya 2,000 ifikapo mwisho wa mradi huu wa msaada wa vyakula,” amesema Piganio.

Baadhi ya wanufaika wa msaada huo wameeleza kufurahishwa na hatua hiyo, wakipongeza juhudi zinazofanywa na Mati Super Brands Ltd kupitia taasisi yake ya Mati Foundation kwa kuwakumbuka wananchi wenye uhitaji, hususan wale wanaoishi katika maeneo yanayozunguka kiwanda hicho.

Wanufaika hao wamesema msaada wa vyakula walioupokea utawapunguzia kwa kiasi kikubwa changamoto za kimaisha, hasa katika kipindi cha ugumu wa upatikanaji wa mahitaji ya msingi, na wameishukuru kampuni hiyo kwa moyo wa kujali na kugusa maisha ya wananchi wa kawaida.

Viongozi mbalimbali wa Serikali waliokuwa mashuhuda wa zoezi hilo wameipongeza Mati Foundation kwa moyo wa kujitolea na ushirikiano wake na Serikali katika kutatua changamoto za kijamii, wakisema mchango huo ni mfano mzuri wa sekta binafsi kushiriki katika maendeleo ya jamii.

Viongozi hao wamesisitiza kuwa ushirikiano wa aina hiyo unasaidia kuimarisha ustawi wa jamii na kupunguza mzigo kwa Serikali katika kuwahudumia wananchi wenye uhitaji.

Mati Foundation ni taasisi isiyo ya kiserikali iliyo chini ya kampuni mama Mati Super Brands Ltd, inayojihusisha na uzalishaji na usambazaji wa vinywaji changamshi mbalimbali nchini. Miongoni mwa bidhaa zinazozalishwa na kampuni hiyo ni pamoja na Strong Dry Gin, Sed Pineapple Flavoured Gin, Strong Coffee, Tai Original Portable Spirit, Tanzanite Premium Vodka na Tanzanite Royal Gin.

Kupitia Mati Foundation, kampuni hiyo imeendelea kutekeleza programu mbalimbali za kijamii zenye lengo la kuinua ustawi wa jamii na kuchangia maendeleo endelevu katika maeneo inayofanyia shughuli zake.




 

Na Mwandishi Wetu

Mkurugenzi wa Wasafi Media, Naseeb Abdul maarufu Diamond Platnumz, ameipongeza Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) kwa kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, huku akiahidi kuwa vyombo vyake vya habari viko tayari kufuata kikamilifu matakwa yote ya kisheria yanayoongoza sekta ya habari nchini.

Diamond ametoa kauli hiyo baada ya kufika katika ofisi za Bodi ya Ithibati kwa ajili ya kupata ufafanuzi wa masuala mbalimbali yanayohusu utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari, akisema Wasafi Media haina nia ya kukwepa sheria bali ina dhamira ya kushirikiana kwa karibu na wasimamizi wa taaluma ya uandishi wa habari.

Amesema licha ya Sheria hiyo kuleta changamoto kwa baadhi ya vyombo vya habari na watumishi wake, bado haiwezi kupingwa kwani ilitoa muda wa kutosha kwa wadau wote kujipanga na kutimiza vigezo vilivyowekwa, ikiwemo sharti la waandishi wa habari kuwa na kiwango cha elimu cha kuanzia Diploma na kuendelea.
Diamond amekiri kuwa kuanzishwa kwa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari kumeleta nidhamu na uwajibikaji mkubwa katika taaluma ya habari, akisisitiza kuwa Wasafi Media inaunga mkono juhudi za Serikali za kuhakikisha weledi, maadili na heshima ya taaluma hiyo inalindwa.

“Sisi hatutaki kukwepa utekelezaji wa Sheria. Hakuna namna unaweza kuvunja Sheria na ukabaki salama. Tumehakikisha watumishi wetu wote wanazingatia Sheria na katika hilo sina utani,” amesema Diamond.

Aidha, amesema hapo awali alipata taarifa na tafsiri tofauti kuhusu Sheria ya Huduma za Habari, hali iliyosababisha sintofahamu kwa baadhi ya wadau, lakini baada ya kufika katika ofisi za Bodi na kupewa ufafanuzi wa kina, ameelewa vyema dhamira ya Serikali ya kuimarisha taaluma ya habari nchini.

Amepongeza pia msimamo wa Waziri mwenye dhamana aliyesisitiza kuwa Bodi ya Ithibati ni mlezi wa waandishi wa habari, akisema baada ya mazungumzo na uongozi wa Bodi, ameridhishwa kuwa taasisi hiyo ipo kwa ajili ya kulinda na kukuza taaluma hiyo, si kuibana.
“Nakiri wazi kuwa Bodi ni mlezi kwa waandishi wa habari. Baada ya kuielewa Sheria vizuri, hakuna sababu ya kupingana nayo. Watu wangu tayari wamechukua hatua stahiki na wamerejea vyuoni kujiendeleza kielimu,” amesema Diamond, akisisitiza umuhimu wa mawasiliano mazuri kati ya wadau wa sekta ya habari na wasimamizi wa Sheria.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, Wakili Patrick Kipangula, amesema Sheria ya Huduma za Habari ilitungwa mwaka 2016 na Serikali ilitoa kipindi cha mpito cha miaka mitano kwa waandishi na taasisi za habari kutimiza matakwa ya kisheria.

Ameeleza kuwa kipindi hicho kiliongezwa kwa miaka miwili na baadaye miaka mingine mitatu, hivyo kufikisha jumla ya miaka kumi, muda ambao Serikali inaamini ulikuwa wa kutosha kwa wadau wote wa sekta ya habari kujiandaa na kutekeleza Sheria hiyo kikamilifu.

Wakili Kipangula amesema utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari unalenga kujenga sekta ya habari yenye weledi, maadili na heshima, sambamba na kulinda maslahi ya waandishi, vyombo vya habari na jamii kwa ujumla.
-Yasaini Mikataba 23 siku 100 za Rais Samia Madarakani.

Dar es Salaam Meneja wa TARURA Mkoa wa Rukwa Mhandisi Chacha Mwita Moseti ameelezea mafanikio waliyoyapata katika ujenzi wa miundombinu ya barabara mkoani humo katika kipindi cha miaka minne iliyopita.

Hayo ameyasema katika Mkutano wa Mwaka wa Barabara uliofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Maktaba ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, jijini Dar es Salaam.

Amesema mafanikio hayo yamechagizwa na ongezeko la bajeti katika Mkoa huo tangu Serikali ya Awamu ya Sita iingie madarakani ambapo bajeti yao imepanda kutoka bilioni 5 hadi kufikia bilioni 13.5.

"Kimsingi tumekuwa na mafanikio makubwa sana ambayo yametuwezesha kuboresha barabara nyingi tulizokuwa nazo kutokana na ongezeko la bajeti kutoka bilioni 5 hadi bilioni 13.5 ambayo ni bajeti tunayoendelea nayo Sasa" "Ongezeko hilo limetusaidia kuzipandisha hadhi barabara zetu kutoka changarawe na kuwa za lami na kutoka udongo na kuwa za changarawe lakini pia kuna maeneo ya milimani tumejenga barabara za zege".

Mhandisi Moseti ameongeza kuwa ongezeko hilo pia limewawezesha kujenga madaraja mengi ya mawe maeneo yote yaliyokuwa na vikwazo na kusababisha barabara kutopitika kwa urahisi na kuwezesha wananchi kupata huduma ya usafirashaji kwa urahisi.

" Kama mnavyojua Mkoa wa Rukwa unasifika sana kwa kilimo na kabla ya hali hii usafirishaji wa mazao kutoka mashambani kuja sokoni hali ilikuwa sio ya kuridhisha ila baada ya kupata ongezeko la bajeti kwa kweli tumefungua barabara nyingi ambazo Sasa zinawasaidia wananchi kutoa mazao yao shambani na kuleta sokoni kwa urahisi".

Kuhusu siku 100 za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan tangu aingie madarakani katika kipindi chake cha pili, Mhandisi Moseti amesema wamefanikiwa kusaini mikataba 23 yenye thamani ya shilingi bilioni 4.8 na Wakandarasi wameshaanza kazi na kazi zinaendelea.
-Amuelekeza Mkandarasi akamilishe jengo kwa wakati

Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi akagua maendeleo ya ujenzi wa jengo la Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali linaloendelea kujengwa kwenye mji wa Serikali, Mtumba jijini Dodoma.

Ujenzi wa jengo hilo umefikia kiwango cha asilimia 73 na umegharimu jumla ya shilingi bilioni 16 na ili liweze kukamilika zitatumika jumla ya shilingi bilioni 26 na linajengwa kwa fedha za Serikali.

Dkt. Possi amemtaka mkandarasi, SUMA JKT na mshauri elekezi, TBA kuhakikisha kuwa jengo hilo linakamilika kwa kuzingatia viwango na ubora unaotakiwa ili liweze kutumika kwa muda mrefu. Pia, amemwelekeza mkandarasi kuwa kisima cha maji ya ardhini kilichochimbwa kitunzwe ili maji yake yaweze kutumika wakati wa msimu wa kiangazi na matumizi mbali mbali ikiwemo utunzaji wa mazingira ili kuifanya Dodoma kuwa ya kijani.

“Nategemea kupata jengo lenye ubora na viwango vinavyotakiwa ili liweze kutumika kwa muda mrefu kwa lengo la kusogeza huduma karibu na wananchi na kuongeza tija na ufanisi katika mnyororo wa utoaji haki nchini,” amesisitiza Dkt. Possi.

Pia, ameongeza kuwa tunahitaji jengo liishe mapema mwaka huu ili tuhamie Dodoma kwa kuwa Ofisi hii inafanya kazi kwa karibu na Mahakama ya Tanzania ambayo tayari imehamia Dodoma.

Dkt. Possi aliambatana na Menejimeneti ya Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, mwakilishi wa mkandarasi, Meneja Ujenzi Kanda ya Mashariki wa SUMA JKT, Kanali Saul Chiwanga na mwakilishi wa mshauri elekezi, Kaimu Meneja Miradi wa TBA, ndugu Daniel Nkruma.
Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi (wa pili kushoto) akipatiwa maelezo na mkandarasi, Meneja Ujenzi Kanda ya Mashariki wa SUMA JKT, Kanali Saul Chiwanga kuhusu maendeleo ya ujenzi wa jengo la Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali wakati wa ziara yake ya kukagua jengo hilo lililopo Mji wa Serikali, Mtumba, Dodoma.
Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi akitoa maelekezo kwa Kaimu Meneja Miradi wa TBA, ndugu Daniel Nkruma anayesimamia ujenzi wa jengo la Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali wakati wa ziara yake ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa jengo hilo Mji wa Serikali, Mtumba, Dodoma.
Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi akizungumza na mkandarasi, Meneja Ujenzi Kanda ya Mashariki wa SUMA JKT, Kanali Saul Chiwanga kuhusu ujenzi wa jengo la Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali unaoendelea wakati wa ziara yake ya kukagua jengo hilo Mji wa Serikali, Mtumba, Dodoma.

Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi akiangalia ramani ya jengo la Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali alipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa jengo hilo unaoendelea katika Mji wa Serikali, Mtumba, Dodoma
Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi akizungumza na wajumbe wa Menejimenti ya Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, Mkandarasi - Suma JKT na mshauri elekezi, TBA (hawapo pichani) kabla ya ziara yake ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa jengo la Ofisi hiyo unaoendelea katika Mji wa Serikali, Mtumba, Dodoma.
Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, Bi. Asha Hayeshi akitoa maelezo mafupi kuhusu maendeleo ya ujenzi wa jengo la Ofisi hiyo kwa Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi (hayupo pichani) alipotembelea mradi huo katika Mji wa Serikali, Mtumba, Dodoma.
Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi akiwa kwenye picha ya pamoja na wajumbe wa Menejimenti ya Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, Mkandarasi - Suma JKT na mshauri elekezi, TBA baada ya ziara yake ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa jengo la Ofisi hiyo unaoendelea katika Mji wa Serikali, Mtumba, Dodoma.




Muonekano wa jengo la Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali linaloendelea kujengwa katika Mji wa Serikali, Mtumba, Dodoma

Na Kassim Nyaki, Amboni Tanga.

Mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro imeshiriki na kudhamini mbio za AmbonI Adventure run zilizofanyika leo tarehe 31 Januari 2026 jijini Tanga kwa lengo la kutangaza vivutio vya utalii hususan mapango ya Amboni yanayosimamiwa na Mamlaka yah ifadhi ya Ngorongoro

Mbio hizo za umbali wa kimomita 6, 10 na 20 ambazo zimehudhuriwa na wakimbiaji zaidi ya 500 kutoka maeneo mbalimbali nchini zimeanzia katika viwanja vya Shule ya Sekondari Galanos hadi Mapango ya amboni ambapo washiriki wa mbio hizo wamepata fursa ya kufanya utalii wa ndani katika mapango hayo.

Kaimu meneja uhusiano wa Ngorongoro Hamis Dambaya ambaye ameshiriki mbio hizo kwa kukimbia kilomita 10 ameeleza kuwa  Ngorongoro imeamua kuungana na wadau mbalimbali kuendelea kutangaza vivutio vilivyoko katika mapango ya Amboni ili yaendelee kujulikana kitaifa na kimataifa na kuvutia wageni wengi kutembelea na kuona vivutio vinavyopatikana katika mapango hayo na kupataa taarifa mbalimbali ikiwemo historia ya wapigania uhuru. 

Msimamizi wa Mapango ya Amboni Afisa Uhifadhi Daraja la kwanza Ramadhan Rashid ameeleza kuwa baadhi ya vivutio vinavyopatikana katika Mapango ya Amboni  ni pamoja na maumbo ya asili ya kijiolojia, vivutio vilivyochongwa na maji kama meli, mlima Kilimanjaro, kanisa, msikiti, shughuli za kimila na mataambiko, ndege ndani ya mapango, pango la jinsia, Pango la fatuma ambalo watu hulitumia kuomba mchumba wa kuoa, mimea ya aina mbalimbali, mto pamoja na mazingira asilia yanayopaambwa naa upepo mwanana wa bahari ya hindi.

Mkuugenzi wa Kale Amboni Caves Sophia Mulamula ameeleza kuwa Mbio za Amboni Adventure Run ambazo zimefanyika kwa msimu wa tatu na kuhudhuriwa na wakimbiaji takriban 500 zinatendelea kuboreshwa ili kuvutia wakimbiaji wengi zaidi mwaka ujao 2027 

“Tumefanya tathmini kwa miaka hii miwili tumeona mbio hizi zinavutia watu wengi, tunaamini mwakani tunaboresha vitu vingi zaidi ili tupate wakimbiaji wengi kwa lengo la kutangaza vivutio vya utalii, kutangaza nchi yetu lakini kuendelea kuhamasisha utalii wa michezo” alilisitiza Mulamula.











 


Top News






Back To Top