‎Chamwino, Dodoma

‎Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) wilaya ya Chamwino imefungua barabara ya Manda–Mafurungu yenye urefu wa kilomita 25 hatua ambayo imebadili hali ya usafiri na usafirishaji kwa wananchi wa kijiji cha Mafurungu baada ya kukabiliwa na changamoto ya muda mrefu ya kutokuwa na barabara.

‎Akizungumza kuhusu maendeleo ya mradi huo, Meneja wa TARURA wilaya ya Chamwino Mhandisi Richard Sanga amesema, barabara hiyo imefunguliwa ikiwa ni jitihada za serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuunganisha wananchi na kurahisisha shughuli za kiuchumi na kijamii.

‎Amesema TARURA wilaya ya Chamwino inahudumia mtandao wa barabara wenye urefu wa kilomita 1,297 huku ujenzi wa barabara ya Manda–Mafurungu ukiwa ni muhimu kwa wananchi wa vijiji vya Manda na Mafurungu kwa ajili ya kurahisisha upatikanaji wa huduma za afya na elimu, kupunguza gharama za usafiri na kufungua fursa za kiuchumi.

‎"Awali barabara hii haikuwepo kabisa lakini baada ya kupata fedha tumeweza kuifungua, mkandarasi tayari ameshafungua kilomita zote 25 huku kazi zinazoendelea ni ujenzi wa makalavati, uwekaji wa kifusi katika maeneo korofi na maandalizi ya uchongaji wa mifereji kwa ajili ya kudhibiti na kuondoa maji ya mvua barabarani", amesema.

‎Ameeleza kuwa kutokana na umuhimu wa barabara hiyo katika bajeti ya mwaka huu wa fedha wataweka changarawe katika baadhi ya maeneo korofi huku mpango wa mwaka ujao wa fedha ukiwa ni kuweka kifusi barabara yote na kumalizia makalavati ili kuhakikisha barabara inapitika kwa urahisi na kwa uhakika kipindi chote cha mwaka.

‎Kwa upande wake, Mwenyekiti wa kitongoji cha Machimbo, Bw. Mrisho Ally amesema kabla ya barabara hiyo wananchi wa Mafurungu wakitaka kusafiri hadi Dodoma mjini safari ya kwenda na kurudi walikuwa wakitumia nauli zaidi ya Sh. 100,000/= hali iliyowalazimu kutumia muda mwingi na gharama kubwa.

‎Amesema kwa sasa gharama hiyo imeshuka hadi Sh. 24,000/= kwa safari ya kwenda na kurudi huku magari yakiwa yanafika moja kwa moja kijijini ambapo imepunguza gharama na muda wa usafiri.

‎Ameongeza kuwa eneo hilo lina shughuli kubwa za uchimbaji wa madini ya dhahabu zinazochangia uchumi wa wilaya ya Chamwino hivyo ameiomba serikali kuendelea kuboresha barabara hiyo ili iweze kutoa huduma kwa wananchi na wafanyabiashara katika kipindi cha mwaka mzima.

‎Naye, Bw. Zabroni Matonya mkazi wa Mafurungu na mwekezaji katika shughuli za uchimbaji madini amesema, barabara hiyo imekuwa mkombozi kwa wachimbaji na wawekezaji kutokana na kurahisisha usafirishaji wa vifaa na malighafi kwani awali ubovu wa barabara uliwafanya kutumia muda mrefu kusafirisha malighafi zao mjini hivyo ameishukuru serikali kwa barabara hiyo.

‎Mkazi wa Mafurungu Bi. Salma Mtacha amesema kabla ya barabara wanafunzi walikuwa wakitembea umbali mrefu kufika shuleni hali iliyokuwa ikiwatia hofu wazazi lakini sasa barabara imefunguka wanafunzi wanafika shuleni bila shida pia wananchi wanafika katika vituo vya afya na hospitali bila changamoto jambo ambalo limeongeza usalama na ustawi wa jamii.

‎Naye, Selemani Bundala mkazi wa Mafurungu amesema awali safari ya kutoka kijijini hadi Dodoma mjini kwa pikipiki ilikuwa ikigharimu hadi Sh. 100,000/= lakini baada ya barabara kufunguliwa hali imebadilika na mabasi sasa yanafika moja kwa moja kijijini.

‎Amesema wananchi wanathamini jitihada za serikali katika kufungua barabara hiyo na ameomba kazi ya uboreshaji iendelee hadi barabara hiyo iweze kupitika mwaka mzima.





Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) umeendelea kuvuna matunda ya uwekezaji katika utalii wa misitu, huku idadi ya watalii wanaotembelea vivutio vinavyosimamiwa na taasisi hiyo ikifikia 377,116 mwaka 2025, ikiwa ni ongezeko kubwa kutoka watalii 46,533 mwaka 2020.

Kwa mujibu wa Mkuu wa Kitengo cha Utalii TFS, PCO Someni Mteleka, ongezeko hilo linaenda sambamba na kuimarika kwa mchango wa utalii katika mapato ya taasisi, ambapo mwaka 2020 TFS ilirekodi watalii mapato ya zaidi ya Sh 159 milioni kutokana na utalii wa ikolojia na kuongezeka hadi Sh 3.5 bilioni mwaka 2025/2026

Akizungumza jana Septemba 15, 2026 jijini Dodoma wakati wa mafunzo ya utangulizi kwa watumishi wapya wa TFS, Mteleka alisema taasisi hiyo inaendelea kuendeleza bidhaa mbalimbali za utalii zinazotokana na misitu, mashamba ya miti, mikoko na maeneo ya kihistoria, hatua inayolenga kuongeza fursa za utalii na manufaa ya kiuchumi.

Alisema TFS kwa sasa inasimamia maeneo 35 ya utalii yanayotoa shughuli mbalimbali, zikiwemo matembezi ya misituni, kuangalia ndege na wanyama, kupanda na kutalii milimani, utalii wa nyuki, baiskeli, kuendesha mitumbwi na kayak, kambi, picnic, pamoja na kutembelea maeneo ya kihistoria na kitamaduni.

Mteleka alisema ukuaji wa utalii umechangiwa pia na kuongezeka kwa maeneo ya hifadhi za misitu ya kitaifa (NFRs), ambayo yameongezeka kutoka maeneo matano mwaka 2015 hadi kufikia 25 mwaka 2025, huku utalii wa ikolojia ukiwa miongoni mwa shughuli kuu za kiuchumi zinazoruhusiwa katika maeneo hayo kwa kuzingatia uhifadhi na athari ndogo kwa mazingira.

Alisema mbali na hifadhi za misitu, TFS inaendelea kutumia mashamba ya miti na misitu ya mikoko kuendeleza bidhaa mpya za utalii zisizohitaji uvunaji wa rasilimali, ikiwemo utalii wa michezo kama mbio za magari, marathoni na shughuli za kuendesha farasi, pamoja na shughuli za utalii katika maeneo ya mikoko.

Kwa mujibu wa Mteleka, TFS pia inasimamia vituo sita vya maeneo ya kale, vikiwemo Mji Mkongwe wa Bagamoyo, Magofu ya Kaole, Tongoni, Michoro ya Miamba ya Kondoa ambayo ni eneo la Urithi wa Dunia la UNESCO, pamoja na maeneo yanayohusishwa na Dk. David Livingstone na Jengo la Afya.

Alisema TFS inaendelea kushirikiana na taasisi za Serikali, washirika wa maendeleo, mashirika yasiyo ya Serikali, jamii na sekta binafsi katika kuboresha miundombinu, huduma na upatikanaji wa vivutio, huku ikiendelea kutangaza bidhaa zake kupitia vyombo vya habari vya jadi na kidijitali ili kuongeza watalii na kuchangia lengo la taifa la kufikia watalii milioni nane kwa mwaka ifikapo 2030.






TUMBATU, ZANZIBAR — Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Ndugu Abdi Mahamoud Abdi, amekagua ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Tumbatu, akieleza kuwa kukamilika kwa mradi huo kutarahisisha upatikanaji wa huduma za afya, ikiwemo huduma za kibingwa, kwa wananchi wa Kisiwa cha Tumbatu.

Akitoa taarifa ya kitaalamu wakati wa ziara hiyo, msimamizi wa mradi amesema hospitali hiyo itatoa huduma mbalimbali za afya, zikiwemo huduma za afya ya jamii na huduma za kibingwa, hatua itakayosaidia kupunguza changamoto ya wananchi kusafiri nje ya kisiwa kufuata huduma hizo.

Wananchi wa Tumbatu wamempongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, kwa kuendelea kutekeleza ahadi za Serikali kwa vitendo, hususan katika kuimarisha huduma za kijamii na afya.

Kwa upande wake, Ndugu Abdi amempongeza Dkt. Mwinyi kwa hatua zinazoendelea kuchukuliwa katika kuimarisha huduma za afya katika Kisiwa cha Tumbatu, huku akisisitiza umuhimu wa kukamilisha miradi hiyo kwa wakati ili wananchi waanze kunufaika na huduma zinazotarajiwa.

Aidha, amewataka madaktari na watumishi wa afya kuhakikisha wanatoa huduma bora, zenye weledi na zinazozingatia mahitaji ya wananchi, akisisitiza kuwa lengo la Serikali ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za afya na kuimarisha ustawi wao.

📆 16 Septemba, 2026
📍 Tumbatu, Zanzibar.










 

Na. Asia Singano, WF – Dodoma.

Wizara ya Fedha imeendelea kuandaa na kuboresha miongozo mbalimbali inayolenga kuimarisha utekelezaji wa majukumu ya ukaguzi na kuongeza ufanisi wa kazi hiyo, ili kuendelea kulinda fedha za umma na kukuza uchumi wa nchi.

Hayo yameelezwa na Kaimu Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Wizara ya Fedha, Mhandisi Kenneth Nindie, wakati akifungua Mafunzo ya Uelewa na Ugawaji wa Mwongozo wa Ukaguzi wa Mifumo ya Taarifa kwa Wakaguzi wa Ndani wa Serikali, yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mabele jijini Dodoma.

Mhandisi Nindie alisema kuwa mwongozo huo unahusisha hatua mbalimbali za mchakato wa ukaguzi, na kwamba baadhi ya vipengele vyake vinapitia hatua ya uhakiki ili kuhakikisha vinaendana na mahitaji na viwango vinavyotakiwa.

“Tunachukua baadhi ya vipengele kwa ajili ya kuvithibitisha, ambapo ni muhimu kupitia na kuthibitisha miongozo hiyo kabla ya kuanza kutumika kikamilifu. alisema Mhandisi Nindie.

Alieleza kuwa hatua hiyo inalenga kuhakikisha kuwa miongozo inayotumika katika kazi za ukaguzi ina ubora, inaeleweka na inawasaidia watendaji kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa watumishi kuwa na vyeti vya kitaaluma (certification), kwakuwa hatua hiyo ni muhimu katika kuongeza ufanisi na ubora wa utekelezaji wa majukumu yao.

“Suala la kuwa na vyeti vya kitaaluma limekuwa sehemu muhimu ya mipango ya kuimarisha uwezo wa watumishi. Natambua kuwa tangu mwaka 2021 kulikuwa na mpango uliolenga kuongeza idadi ya watumishi wenye vyeti hivyo,” alisema Mhandisi Nindie.

Alibainisha kuwa kuendelea kuwekeza katika ujuzi na taaluma za watumishi ni hatua muhimu katika kuboresha utendaji kazi na kuhakikisha majukumu ya taasisi yanatekelezwa kwa viwango vinavyohitajika.

Mafunzo hayo yaliandaliwa na Wizara ya Fedha, kupitia Idara ya Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali yakiwakutanisha Wakaguzi wa Ndani kutoka taasisi za umma na kutoka Wizara ya Fedha, ili kuwaongezea uelewa katika utekelezaji wa majukumu yao.


Kaimu Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Wizara ya Fedha, Mhandisi Kenneth Nindie, akizungumza wakati wa kufungua Mafunzo ya Uelewa na Ugawaji wa Mwongozo wa Ukaguzi wa Mifumo ya Taarifa kwa Wakaguzi wa Ndani wa Serikali, yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mabele jijini Dodoma.

Kaimu Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Wizara ya Fedha, Mhandisi Kenneth Nindie (kushoto), akiagana na Mhasibu Mkuu wa Fungu 6 – Idara ya Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Samwel Mangi, baada ya kumalizika kwa Mafunzo ya Uelewa na Ugawaji wa Mwongozo wa Ukaguzi wa Mifumo ya Taarifa kwa Wakaguzi wa Ndani wa Serikali, yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mabele jijini Dodoma.

Kaimu Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Wizara ya Fedha, Mhandisi Kenneth Nindie (kushoto), akijadiliana jambo na Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali Msaidizi, Idara ya Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Paison Mwamnyasi, wakati wa Mafunzo ya Uelewa na Ugawaji wa Mwongozo wa Ukaguzi wa Mifumo ya Taarifa kwa Wakaguzi wa Ndani wa Serikali, yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mabele jijini Dodoma.

Mkaguzi wa Ndani Mwandamizi, Idara ya Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Wizara ya Fedha, Bi. Vaileth Nyanga, akitoa wasilisho kuhusu muhtasari Mifumo ya Kuimarisha Ufanisi wa Kazi za Ukaguzi Serikalini, wakati wa program ya Mafunzo ya Uelewa na Ugawaji wa Mwongozo wa Ukaguzi wa Mifumo ya Taarifa kwa Wakaguzi wa Ndani wa Serikali, yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mabele jijini Dodoma.

Kaimu Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Wizara ya Fedha, Mhandisi Kenneth Nindie, akigawa kitabu cha Mwongozo wa Ukaguzi wa Mifumo ya Taarifa kwa, Mkaguzi wa Ndani kutoka Tume ya Maendeleo ya Ushirika (TCDC), Bw. Ernest Josephat, mmoja wa washiriki wa program ya Uelewa na Ugawaji wa Mwongozo iliyowakutanisha wakaguzi wa ndani kutoka taasisi za umma ambayo yaliandaliwa na Wizara ya Fedha, yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mabele jijini Dodoma.

Kaimu Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Wizara ya Fedha, Mhandisi Kenneth Nindie (katikati, walioketi), na Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali Msaidizi, Bw. Paison Mwamnyasi (wa tatu kushoto, walioketi), wakiwa katika picha ya pamoja na Wakaguzi wa Ndani baada ya Mafunzo ya Uelewa na Ugawaji wa Mwongozo wa Ukaguzi wa Mifumo ya Taarifa kwa Wakaguzi wa Ndani wa Serikali, yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mabele jijini Dodoma.

(Picha na Kitengo Cha Mawasiliano Serikalini, WF – Dodoma)





Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) imeratibu na kuendesha semina mtandao (Webnar) maalum ikilenga kuwahamasisha Watanzania kutumia fursa zinazopatikana katika masoko ya mitaji na hisa nchini hususani kupitia maendeleo ya teknolojia yaliyorahisisha ufikiwaji wa masoko hayo hadi kupitia njia ya simu za mikononi.

Semina hiyo iliyorushwa moja kwa moja mtandaoni kutoka makao makuu ya benki hiyo iliwahusisha wadau tofauti waliowakilisha taasisi wasimamizi ikiwemo Benki Kuu ya Tanzania, Soko la Hisa Dar es Salaam (DSE) na Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA).

Akizungumza katika semina hiyo, ambayo pamoja na mambo mengine ilijadili namna wananchi hususani wa kipato cha chini wanavyoweza kutumia akaunti zao za benki kufikia masoko ya mitaji, Mkurugenzi Mtendaji wa NBC, Theobald Sabi, alisema kwasasa ni wakati muafaka kwa watanzania kutumia taasisi za fedha kama vituo vya elimu kwenye masuala muhimu ya uwekezaji tofauti utamaduni uliojengeka wa taasisi hizo kutumika kama sehemu ya kuweka akiba na mikopo.

“Na hii ndio sababu kama benki tunawekeza zaidi kwenye mifumo inayowawezesha wateja wetu kushiriki katika uwekezaji wa masoko ya mitaji. Yaani kwamba sasa benki ni zaidi ya kuweka akiba na kukopa bali ni kuinganishi muhimu cha elimu na huduma za kuyafikia masoko ya mitaji na soko la hisa,” alisema Sabi.

Alitolea mfano wa huduma ya NBC Kiganjani ambayo imeunganishwa na DSE Kiganjani, huku mifumo ya mifuko ya uwekezaji ya UTT na iTrust nayo ikiwa imeunganishwa na huduma hiyo na huduma nyingine zikiwa katika hatua za kuunganishwa.

Alitoa wito kwa Watanzania wenye fedha kuacha kuzihifadhi bila kuzalisha thamani na badala yake kuzitumia katika fursa mbalimbali za uwekezaji, ikiwemo hisa na hati fungani za Serikali.

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa Soko la Hisa Dar es Salaam (DSE), Peter Nalitolela, alisema safari ya uwekezaji katika masoko ya mitaji si ngumu kama inavyodhaniwa, kutokana na kurahisishwa kwa huduma kupitia simu za mkononi na upatikanaji wa ushauri wa uwekezaji kupitia matawi ya benki.

Alisema licha ya idadi ya wawekezaji kwenye masoko ya mitaji nchini kuongezeka na kufikia takribani 900,000, bado idadi hiyo ni ndogo ikilinganishwa na idadi ya Watanzania inayokadiriwa kufikia zaidi ya milioni 70.

“Naendelea kuwahimiza wananchi kutokuona uwekezaji kama shughuli inayohitaji kuwa na mamilioni ya fedha, na msisitizo wangu kwao ni kwamba mtu yeyote anaweza kuanza kwa kiasi kidogo, ikiwemo Sh5,000 au Sh20,000, kutegemea bidhaa na masharti ya uwekezaji husika.’’ Alisema.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Utafiti, Sera na Mipango wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), CPA Alfred Mkombo, alisema mamlaka hiyo inaendelea kusimamia masoko ya mitaji kwa lengo la kulinda maslahi ya wawekezaji na kuhakikisha wanafanya maamuzi wakiwa na uelewa wa kutosha kuhusu uwekezaji wanaoufanya.

Mkombo aliwashauri wawekezaji kutoweka fedha zao zote katika eneo moja, bali kugawanya uwekezaji katika maeneo mbalimbali kama hati fungani, mifuko ya uwekezaji wa pamoja, nyumba na makazi pamoja na amana za muda maalumu benki.

Naye Emmanuel Akaro, Mkurugenzi wa Masoko ya Fedha kutoka Benki Kuu ya Tanzania (BoT), alisema benki hiyo inaendelea kufanya maboresho yenye lengo la kuongeza wigo wa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi katika masoko ya mitaji.

Alisema kuna fedha nyingi ambazo hazipo kwenye mzunguko wa uchumi na kwamba kuna umuhimu wa kuwa na mikakati ya kuwahamasisha wamiliki wa fedha hizo kuziwekeza katika maeneo kama hati fungani, benki na mifuko ya uwekezaji wa pamoja.

“Tangu mwezi Julai, baada ya mabadiliko ya sheria yaliyofungua akaunti ya mitaji, wawekezaji kutoka nje wakiwemo Diaspora wamewezeshwa kushiriki katika soko la dhamana za Serikali hatua inayowawezesha Watanzania wanaoishi nje ya nchi, ikiwemo wale ambao watoto wao hawana uraia wa Tanzania, kuwekeza katika hati fungani za Serikali na kunufaika na uwekezaji huo.’’ Alisema.

Akizungumzia semina mtandao (Webnar) hiyo, Sarah Laizer Sumaye, Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Udhibiti (Director of Compliance and Regulatory Affairs) wa NBC, alisema ilikuwa sehemu ya mpango endelevu wa benki wa kutoa elimu kwa wateja kuhusu fursa mbalimbali za kifedha.

Alisema webinar hiyo, iliyowakutanisha wataalamu kutoka NBC, DSE, CMSA na BoT, imelenga hasa kumsaidia Mtanzania wa kawaida kuelewa namna anavyoweza kutumia huduma za benki kufikia masoko ya mitaji na kuwekeza kwa ajili ya malengo yake ya kifedha.

“Hatutaishia kwenye akiba na mikopo. Tunataka kuwapa wateja wetu fursa mbalimbali, ikiwemo fursa za uwekezaji endelevu,” alisema.

Sumaye alisema NBC itaendelea na programu hiyo ya elimu kupitia mpango wa Compliance Advocacy Program, ambapo pamoja na masoko ya mitaji, benki hiyo itaendelea kutoa elimu kuhusu maeneo mengine yakiwemo Mazingira, Jamii, na Utawala (ESG), Faragha ya Taarifa (Data Privacy) na Maadili ya Biashara (Business Ethics)
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC (aliyeshika kipaza sauti) akizungumza wakati wa semina mtandao (webinar) maalum iliyoandaliwa na benki hiyo kwa kushirikiana na wadau wa sekta ya fedha. Semina hiyo imelenga kuhamasisha Watanzania kuchangamkia fursa za masoko ya mitaji na hisa nchini, hususan kupitia teknolojia ya simu za mkononi. Waliopo meza kuu kutoka kushoto: Ibrahim Nzutu, Mkuu wa Idara ya Ushauri wa Biashara NBC (Muendesha Semina), Peter Nalitolela, Afisa Mtendaji Mkuu wa Soko la Hisa Dar es Salaam (DSE), Theobald Sabi, Mkurugenzi Mtendaji wa NBC, Emmanuel Akaro, Mkurugenzi wa Masoko ya Fedha, Benki Kuu ya Tanzania (BoT) na Alfred Mkombo, Mkurugenzi wa Utafiti, Sera na Mipango (CMSA)




Afisa Mtendaji Mkuu wa Soko la Hisa Dar es Salaam (DSE), Peter Nalitolela (aliyeshika kipaza sauti) akizungumza wakati wa semina mtandao (webinar) maalum iliyoandaliwa na benki ya NBC kwa kushirikiana na wadau wa sekta ya fedha. Semina hiyo imelenga kuhamasisha Watanzania kuchangamkia fursa za masoko ya mitaji na hisa nchini, hususan kupitia teknolojia ya simu za mkononi. Kulia meza kuu ni Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC, Theobald Sabi na Ibrahim Nzutu, Mkuu wa Idara ya Ushauri wa Biashara NBC (Muendesha Semina)


Mkurugenzi wa Utafiti, Sera na Mipango wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), CPA Alfred Mkombo, (aliyeshika kipaza sauti) akizungumza wakati wa semina mtandao (webinar) maalum iliyoandaliwa na benki ya NBC kwa kushirikiana na wadau wa sekta ya fedha. Semina hiyo imelenga kuhamasisha Watanzania kuchangamkia fursa za masoko ya mitaji na hisa nchini, hususan kupitia teknolojia ya simu za mkononi.


Mkurugenzi wa Masoko ya Fedha kutoka Benki Kuu ya Tanzania (BoT) Emmanuel Akaro, (aliyeshika kipaza sauti) akizungumza wakati wa semina mtandao (webinar) maalum iliyoandaliwa na benki ya NBC kwa kushirikiana na wadau wa sekta ya fedha. Semina hiyo imelenga kuhamasisha Watanzania kuchangamkia fursa za masoko ya mitaji na hisa nchini, hususan kupitia teknolojia ya simu za mkononi.


Baadhi ya washiriki wa semina hiyo wakiwemo maofisa waandamizi wa benki ya NBC, CMSA, BOT na DSE wakifuatilia mijadala kutoka kwa wawasilishaji.


Akizungumzia semina mtandao (Webnar) hiyo, Sarah Laizer Sumaye (alieshika mic) ambaye Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Udhibiti (Director of Compliance and Regulatory Affairs) wa NBC, alisema ilikuwa sehemu ya mpango endelevu wa benki wa kutoa elimu kwa wateja kuhusu fursa mbalimbali za kifedha.


Semina hiyo iliyorushwa moja kwa moja mtandaoni kutoka makao makuu ya benki ya NBC iliwahusisha wadau tofauti waliowakilisha taasisi wasimamizi ikiwemo Benki Kuu ya Tanzania (BOT), Soko la Hisa Dar es Salaam (DSE) na Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA).



Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Ndugu Abdi Mahamoud Abdi, amewasili katika Kisiwa cha Tumbatu, Jimbo la Tumbatu, kuendelea na ziara yake ya kukagua na kuimarisha uhai wa Chama Cha Mapinduzi katika matawi.

Ziara hiyo inalenga kukutana na wanachama, kusikiliza changamoto zinazowakabili, pamoja na kuhimiza mshikamano, utekelezaji wa majukumu na uimarishaji wa Chama katika ngazi za chini.















WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema ndani ya wiki moja, Serikali itachukua hatua ya kuhakikisha bei ya saruji inakuwa himilivu kwa wananchi, baada ya kubaini malalamiko ya kupanda kwa bei ya bidhaa hiyo katika mikoa mbalimbali nchini ikiwemo Simiyu.

Ametoa kauli hiyo jana (Jumanne, Septemba 15, 2026) wakati akizungumza na wananchi wa Bariadi Mjini, mkoani Simiyu katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye viwanja vya CCM Saba Saba.

“Serikali tumeliona hilo. Serikali sikivu tumesikia hilo. Nimewatuma wataalamu ndani ya wiki moja wawe wameshapata ufumbuzi. Tutatoa tamko la njia ya kushusha bei ya saruji ili kila Mtanzania aweze kumudu. Katika baadhi ya maeneo bei ya saruji imefikia zaidi ya sh. 26,000 na katika baadhi ya mikoa ya mipakani imefikia sh. 32,000,” amesema na kusisitiza kuwa Serikali inataka wananchi waweze kumudu gharama za ujenzi wa nyumba na miradi mingine ya maendeleo.

Kuhusu zao la pamba, Waziri Mkuu amesema ameielekeza Wizara ya Kilimo ikutane na wadau wa pamba ndani ya mwezi mmoja na ifikapo Oktoba 15, 2026 apelekewe mapendekezo rasmi kuhusu bei na mfumo bora wa ununuzi wa zao hilo ili kuhakikisha wakulima wananufaika zaidi.

“Nimeipokea hoja hii. Nimeelekeza Wizara ya Kilimo ikae na wadau wa pamba ndani ya mwezi mmoja. Ifikapo tarehe 15 mwezi wa 10, niwe nimeshapata mapendekezo rasmi yaliyorejea mifumo ambayo tumeshaitumia na kubaini upi ni mfumo bora ili tuweze kuhakikisha kwamba wakulima wananufaika,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema pia Serikali imebadilisha utaratibu wa kodi kwa wenye biashara mpya, ambapo mfanyabiashara anayeanzisha biashara atapewa muda wa kuimarisha biashara yake kabla ya kuanza kubeba mzigo wa kodi. “Zamani ilikuwa mtu akianzisha tu biashara, siku hiyo hiyo anaanza kudaiwa kodi. Sasa tumefuta, atasubiriwa mwaka mzima ili biashara yake iimarike,” amesema.

Amesema hatua hizo ni sehemu ya utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya 2050 inayolenga kujenga uchumi shirikishi, ambapo sekta binafsi inatarajiwa kutekeleza sehemu kubwa ya shughuli za maendeleo.

Mapema, akizungumza katika mkutano huo, Mbunge wa Bariadi Mjini ambaye pia ni Naibu Waziri wa Maji, Mhandisi Kundo Andrea Mathew, amemshukuru Waziri Mkuu kwa ziara hiyo na kueleza kuwa Serikali imeendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika jimbo hilo ikiwemo inayogusa sekta za maji, elimu, afya na barabara. 

Mhandisi Kundo amesema mradi mkubwa wa maji kutoka Ziwa Victoria wenye thamani ya sh. bilioni 440 unaendelea kutekelezwa mkoani humo, huku Serikali ikiwa imetoa sh. milioni 460 kupitia TARURA kwa ajili ya ujenzi wa daraja la Majaida–Munambala katika Mto Ndoba.

Kuhusu ujenzi wa soko la kisasa la Bariadi mjini, Mhandisi Kumndo amesema ujenzi wake unaendelea, huku akiomba kasi ya mkandarasi iongezwe ili mradi huo ukamilike kwa wakati.

Akigusia barabara za Bariadi Mjini, Mhandisi Kundo amesema Serikali imeweka mpango wa kuhakikisha kilomita zote 8.6 zilizotengewa ujenzi zinajengwa kwa awamu mbili, ambapo kilomita tano zitajengwa katika awamu ya kwanza.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Said Mtanda, amesema Serikali ya Mkoa itasimamia na kutekeleza maelekezo yote yaliyotolewa na Waziri Mkuu wakati wa ziara hiyo na kuwasilisha taarifa ya utekelezaji katika Ofisi ya Waziri Mkuu.

“Maagizo na maelekezo yako uliyoyatoa katika ziara yako hii tunayasimamia, tuyatekeleze, na kuleta ripoti ya utekelezaji katika ofisi yako ya Waziri Mkuu,” amesema.










Top News