Na Mashaka Mhando, Tanga

Hatimaye, Mzee Mohamed Rashid Mkwaje, ambaye aliondoka nyumbani kwao tangu mwaka 1974 kwenda kufanya kazi ya kukata mkonge wilayani Muheza, amefanikiwa kurejea na kuungana tena na familia yake katika Kijiji cha Ligunga, wilayani Tunduru mkoani Ruvuma, baada ya kupita miaka 52.

Mzee huyo amepokelewa kwa hisia kali na vilio vya furaha, hasa kutoka kwa mama yake mzazi, Asmin Kandulu ambaye alikuwa amekata tamaa na kutokuwa na uhakika kama mwanaye alikuwa bado hai baada ya ukimya wa zaidi ya nusu karne.

Kufuatia mapokezi hayo, wajukuu na ndugu wengine wa familia walimfanyia matambiko maalum ya kimila yaliyoambatana na nyimbo za asili za kabila la Kihiyao, ikiwa ni ishara ya kumpokea na kusherehekea kurejea kwa mtoto wao aliyekuwa amepotea.

Safari ya kurejea kwa Mzee Mkwaje ilianza Alhamisi Augosti 20 akitokea Wilaya ya Muheza mkoani Tanga, ambapo alisindikizwa na Ofisa Ustawi wa Jamii wa wilaya hiyo, Silvanus Misigaro.

Akizungumza baada ya kufanikisha safari hiyo, Misigaro alisema walimkabidhi mzee huyo kwa Mganga Mkuu wa Wilaya ya Tunduru Alfred Rwechungura pamoja na Ofisa Ustawi wa eneo hilo, ambao walishirikiana kumfikisha hadi kijijini kwao Ligunga.

"Alipokelewa na mama yake mzazi Asmina, kiukweli mama yake alilia sana kwa kumkosa mtoto wake kwa miaka mingi. Alikuwa na hisia sana na hakuwa na uhakika kama mwanaye huyu bado alikuwa hai," alisema Misigaro akisimulia tukio hilo la kusisimua.

Awali, Mzee huyo ambaye alikuwa akiishi Kijiji cha Ngomeni wilayani Muheza bila familia yoyote, alifika katika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Muheza kuomba msaada wa nauli ya kumrudisha kwao. Kufuatia maombi hayo, ofisi hiyo ilimpatia kibali maalum cha kuchangisha fedha za hiari (Kumb. Na. DC/MUH/S.20/VOL. VIII/232) kilichoanza kutumika Agosti 10 mwaka huu.

Hata hivyo, wakati Mzee Mkwaje akiwa amefanikiwa kuchangisha kiasi cha Shilingi 30,000 pekee kupitia kibali hicho, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Balozi Dkt. Batilda Burian, aliguswa na mkasa huo na kutoa msaada wa Shilingi 200,000 kwa ajili ya nauli, fedha zilizokabidhiwa kupitia kwa Mwandishi wa Habari, Mashaka Mhando, ambaye naye alimkabidhi Ofisa Ustawi, Misigaro.

Akizungumza kwa furaha baada ya kufika nyumbani na kuonana na wapendwa wake, Mzee Mkwaje alitoa shukrani za dhati kwa Serikali ya Wilaya ya Muheza na Tunduru, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, na watu wote waliojitolea kwa namna moja au nyingine kuhakikisha anatimiza ndoto ya kuonana tena na mama yake tangu alipoondoka kwenda kwenye mashamba ya mkonge miongo mitano iliyopita.

"Naishukuru serikali kusema kweli, wameniheshimisha, sikuwa nina uhakika kama kweli nitarudi nyumbani, niliona kama jambo ambalo haiwezekani kutokana na kwamba nilikuwa naona sieleweki ombi nililokuwa nataka kurudi nyumbani, nawashukuru wote waliohusika na hili," alisema.




-HAPI AKUTANA NA RAIS DANIEL CHAPO WA MSUMBIJI, AWASILISHA SALAMU ZA MWENYEKITI WA CCM RAIS DKT. SAMIA SULUHU HASSAN

Chimoio, Msumbiji — Agosti 22, 2026.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Wazazi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Comrade Ally Salum Hapi, amekutana na kufanya mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Msumbiji ambaye pia ni Rais wa Chama cha FRELIMO, Mhe. Daniel Francisco Chapo.

Mazungumzo hayo yamefanyika jijini Chimoio, Msumbiji, wakati Comrade Hapi akimwakilisha Katibu Mkuu wa CCM, Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro, katika Kongamano la 11 la Kitaifa la Makada wa FRELIMO linaloongozwa na Rais Daniel Chapo.

Kongamano hilo ni sehemu ya maandalizi kuelekea Mkutano Mkuu wa Chama cha FRELIMO unaotarajiwa kufanyika mwaka 2027.

Katika mazungumzo hayo, Comrade Hapi amewasilisha salamu za kheri, udugu na ushirikiano kutoka kwa Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa Rais Chapo na chama cha FRELIMO.

Hapi amesema uhusiano kati ya CCM na FRELIMO ni wa kihistoria na wa kindugu, uliyojengwa tangu enzi za harakati za ukombozi wa Afrika, na umeendelea kuimarika katika nyanja mbalimbali.

Chama cha FRELIMO kilianzishwa jijini Dar es Salaam, Tanzania, tarehe 25 Juni 1962, wakati Tanzania ikiwa kitovu muhimu cha harakati za ukombozi wa mataifa ya Kusini mwa Afrika.

Uhusiano huo wa kihistoria umeendelea kuwa msingi muhimu wa ushirikiano kati ya Tanzania na Msumbiji, pamoja na vyama vya CCM na FRELIMO, katika kuendeleza mshikamano, amani na maendeleo ya wananchi wa nchi hizo mbili.

Mazungumzo ya Hapi na Rais Chapo yanaongeza msukumo katika kuendeleza uhusiano wa karibu kati ya vyama hivyo viwili vya ukombozi na kuimarisha ushirikiano wao kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.





Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, amefanya ziara ya kushtukiza katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mwananyamala, jijini Dar es Salaam, kwa lengo la kukagua hali ya utoaji wa huduma kwa wananchi.

Waziri Mkuu amefanya ziara hiyo leo Jumapili, Agosti 23, 2026, ambapo baada ya kuwasili hospitalini hapo ametembelea wodi mbalimbali, zikiwemo Wodi ya Mama na Mtoto pamoja na Wodi ya Upasuaji.

Akiwa katika wodi hizo, Dkt. Nchemba amezungumza na wagonjwa pamoja na ndugu zao, kusikiliza maoni yao kuhusu huduma wanazopata na kufahamu changamoto zinazowakabili wakati wa kupata matibabu.

Wananchi waliokutana na Waziri Mkuu wamempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na Serikali kwa juhudi zinazoendelea katika kuboresha huduma za afya na mazingira ya utoaji wa huduma hospitalini.

Ziara hiyo imefanyika ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali za kufuatilia kwa karibu utoaji wa huduma za kijamii na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora, kwa wakati na katika mazingira yanayokidhi mahitaji yao.

Katika ziara hiyo, Waziri Mkuu ameambatana na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila; Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Mhe. Saad Mtambule; pamoja na viongozi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mwananyamala.







Kamishana wa kamisheni ya Polisi Jamii nchini, CP Alex Mkama amewataka maafisa, wakaguzi na askari wa vyeo mbalimbali wa Jeshi la Polisi kuendelea kuzingatia maadili na kudumisha nidhamu wanapotekelezaji wa majukumu yao ili kujenga uhusiano mzuri na jamii. Pia amewataka kutofanya kazi kwa mazoea kutokana na mabadiliko ya kasi ya uhalifu.

CP Mkama ametoa maagizo hayo leo Jumamosi Agosti 22, 2026, wakati wa maadhimisho ya miaka 15 ya utumishi wa umoja wa askari wa Jeshi la Polisi waliohitimu depo mwaka 2011/2012 (GH Tanzania) huku akidokeza kuwa wananchi wamekuwa wakilalamikia maadili ya baadhi ya maafisa wakaguzi na askari.

“Askari lazima awe na maadili wakati wote. Wananchi wamekuwa wakilalamikia maadili ya baadhi ya maafisa wakaguzi na askari, hivyo ili tuwe na mahusiano mazuri na wananchi lazima maadili yawe mazuri. Tuyaenzi maadili ya afisa wa polisi,” amesema Cp Mkama 

Amesema nidhamu ni msingi wa jeshi lolote duniani, akiwataka askari kuhakikisha wanazingatia misingi hiyo wakati wote huku akidokeza kuwa mabadiliko ya dunia yamechangia kubadilika kwa mbinu za uhalifu.

Awali, akiwasilisha hotuba ya GH Tanzania, mlezi wa kundi hilo, ASP Mabuba Malima amesema umoja huo umeendelea kujikita katika kusaidiana wakati wa changamoto na kurudisha kwa jamii.

Amesema wanachama hao wa GH Tanzania wametoa msaada wa zaidi ya Sh11 milioni kwa watoto wanaosoma katika Shule ya Wanafunzi Wenye Mahitaji Maalum ya Mitindo wilayani Misungwi, yakiwemo madawati 53, magodoro 100, mashuka 200, mchele kilo 200, mafuta ya kupikia lita 60, debe moja la maharage pamoja na mahitaji mengine muhimu.

Malima amesema GH Tanzania ilianzishwa na wanachama wa depo ya mwaka 2011/2012 baada ya kutawanywa katika vituo mbalimbali vya kazi Machi 30, 2012, ikianza na wanachama 75 na sasa ikiwa na zaidi ya wanachama 1,500 Tanzania Bara na Visiwani.

“Wanachama walianza kwa kuchangishana Shilingi 5,000 pekee, lakini kwa sasa umoja huo umekuwa ukitoa zaidi ya Sh7 milioni kwa mwanachama anayepatwa na msiba wa mzazi, mtoto au mwenza,” amesema Malima.

Aidha, amesema zaidi ya Sh15 milioni hutolewa kwa ndugu wa mwanachama aliyefariki au mwanachama anayefukuzwa kazi ili kumsaidia kujikimu huku kila ifikapo Agosti 15, wanachama hao hutenga muda wa kufanya shughuli za kijamii badala ya kusherehekea peke yao, zikiwemo kutembelea wagonjwa hospitalini, kufanya usafi katika masoko na stendi, kutembelea vituo vya watu wenye mahitaji maalum pamoja na kushiriki michezo na burudani.

Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo cha Polisi Wanamaji Mwanza, SACP Ndagile Makubi amesema maboresho yanayoendelea ndani ya Jeshi la Polisi yanaonekana kupitia ushirikiano wa askari katika shughuli mbalimbali za kijamii.







Na Belinda Joseph – Tanga

Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) kimesema matumizi ya teknolojia katika utoaji wa elimu yamewezesha wanafunzi kusoma, kufanya mawasilisho na kupata huduma za kitaaluma bila kulazimika kusafiri hadi chuoni, hatua inayopanua fursa ya elimu kwa watu waliopo ndani na nje ya Tanzania.

Akizungumza Agosti 23, 2026 katika Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea Tanga, Mkurugenzi wa Huduma za Wanafunzi wa OUT, Dkt. Rwejuna Zacharia, amesema chuo hicho kinatumia mifumo ya kidijitali kurahisisha upatikanaji wa vifaa vya kujifunzia, mihadhara, mitihani, matokeo na mawasiliano kati ya wanafunzi na wahadhiri.

Amesema teknolojia hiyo imewasaidia pia wanafunzi waliopo nje ya Tanzania kushiriki katika mawasilisho ya kitaaluma kupitia Zoom pamoja na wahadhiri na wataalamu waliopo katika maeneo mbalimbali, bila kutumia gharama za kusafiri kwa ajili ya shughuli hizo.

Kwa upande wake, Mratibu wa Ubunifu wa OUT na mwakilishi wa Mkuu wa Chuo, Dkt. Straton Ruhinda, amesema matumizi ya teknolojia ni sehemu ya mabadiliko makubwa katika namna elimu inavyotolewa, akisisitiza kuwa ubunifu haupaswi kuangaliwa kama matumizi ya teknolojia pekee, bali pia namna ya kurahisisha elimu na kuifanya iendane na mazingira ya mwanafunzi.

Amesema OUT inaendelea kuboresha baadhi ya mitaala na programu zake, huku ikitoa elimu kuanzia ngazi ya cheti na diploma hadi shahada za kwanza, uzamili na uzamivu (PhD), kwa kutumia mifumo inayompa mwanafunzi unafuu katika namna ya kufuatilia masomo.

Dkt. Ruhinda amesema mfumo huo umekuwa muhimu kwa wanafunzi wenye majukumu mengine, kwa kuwa unaweza kuwawezesha kufuatilia masomo kwa njia inayolingana na mazingira yao badala ya kulazimika kufika darasani kila siku.

Aidha, amesema OUT imeendelea kutumia teknolojia katika mawasiliano kati ya wanafunzi na wasimamizi wa masomo, ambapo mwanafunzi anaweza kutuma kazi yake kwa njia ya mtandao, kupata mrejesho wa mhadhiri na kuendelea na hatua zinazofuata bila kusafiri.

Dkt. Ruhinda amewakaribisha wananchi wenye nia ya kujiendeleza kielimu kutumia fursa zinazotolewa na Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT), akisema chuo hicho kinatoa programu mbalimbali kuanzia ngazi ya cheti, hadi uzamivu (PhD), huku mfumo wake wa elimu kwa njia ya masafa ukimwezesha mwanafunzi kusoma akiwa katika eneo alilopo na kuendelea na majukumu yake ya kila siku.

Ushiriki wa Chuo kikuu huria cha Tanzania katika Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayofanyika Tanga kuanzia Agosti 15 hadi 24, 2026, unalenga kuwafahamisha wananchi kuhusu programu na fursa mbalimbali zinazotolewa na chuo hicho pamoja na namna elimu kwa njia ya masafa inavyoweza kumfikia mwanafunzi akiwa katika eneo alilopo.







Wananchi wa Mkoa wa Geita wametakiwa kuendelea kudumisha na kuimarisha ushirikiano uliopo kati ya Jeshi la Polisi Jamii na wananchi, ili kupunguza uhalifu katika maeneo mbalimbali mkoani humo.

Wito huo umetolewa leo Agosti 22, 2026 wakati wa maadhimisho ya miaka 20 tangu kuanzishwa kwa mfumo wa Polisi Jamii nchini, yaliyofanyika katika Viwanja vya CCM Kalangalala mjini Geita.=

Akizungumza katika maadhimisho hayo, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhe. Martin Shigela, amesema ushirikiano baina ya wananchi na polisi umekuwa na mchango mkubwa katika kurahisisha mapambano dhidi ya uhalifu mkoani Geita.

"Ushirikiano huu ndio unaotufanya tuweze kupambana na uhalifu kwa urahisi. Tunaposhirikiana, taarifa zinafika kwa wakati na hivyo tunazuia uhalifu kabla haujafanyika," amesema Shigela.

Katika hatua nyingine, Mkuu wa Mkoa amezindua rasmi "Polisi Jamii Run Club mpya ya Mkoa wa Geita. 

Klabu hiyo itakuwa na jukumu la kuhamasisha wananchi kushiriki mazoezi ya kukimbia mbio nyepesi, huku ikiwa na lengo la kuimarisha zaidi uhusiano na ushirikiano kati ya askari na jamii.

Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita,  Safia Jongo, amekiri kuwepo kwa ushirikiano mkubwa kati ya wananchi na jeshi la polisi tangu kuanzishwa kwa falsafa ya Polisi Jamii.

Tumekuwa na ushirikiano mkubwa na jeshi la polisi. Leo hii polisi haogopewi tena mtaani kama zamani ambapo alitumika kutishia watoto. Sasa askari na wananchi ni marafiki katika kulinda usalama," amesema Jongo.

Naye Mratibu wa Polisi Jamii Mkoa wa Geita, Amina Kaando, amesema michezo hiyo inalenga kuunganisha jamii na askari ili wananchi waweze kutambua kuwa askari na jamii ni kitu kimoja katika kuzuia na kupambana na uhalifu.

Maadhimisho ya miaka 20 ya Polisi Jamii Mkoa wa Geita yamedhaminiwa na Mgodi wa Dhahabu GGML. 

Katika maadhimisho hayo, GGML wamefanikiwa kuwakaribisha washiriki wa Jogging kutoka mikoa mingine ikiwemo Kigoma, Shinyanga na Mwanza.










Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewataka viongozi katika ngazi mbalimbali za Serikali kuanza mara moja maandalizi ya kukabiliana na mvua kubwa zinazotarajiwa kunyesha nchini katika kipindi kijacho.

Rais Samia amesema utabiri wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) unaashiria uwezekano wa kuwepo kwa mvua kubwa, hivyo amewataka wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya pamoja na viongozi wa taasisi kuhakikisha maeneo yao yanaweka mikakati madhubuti ya kupunguza athari zinazoweza kujitokeza.

Agizo hilo limetolewa leo, Agosti 22, 2026, wakati Rais Samia akizindua rasmi Mradi wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere (JNHPP) uliopo Rufiji, mkoani Pwani.

Amesisitiza umuhimu wa maandalizi ya mapema, akieleza kuwa viongozi wanapaswa kuhakikisha mifumo ya kukabiliana na majanga iko tayari, huku miundombinu inayoweza kuathiriwa na mvua ikiwekewa ulinzi na hatua stahiki za kuzuia madhara zikichukuliwa kabla ya mvua kuanza.

Kwa mujibu wa Rais Samia, maandalizi hayo yanapaswa kuhusisha ushirikiano wa karibu kati ya Serikali na wananchi ili kuongeza uwezo wa kukabiliana na majanga, kulinda maisha ya watu, mali pamoja na miundombinu muhimu.

Aidha, amewataka wananchi kutopuuza tahadhari zinazotolewa na mamlaka husika, bali kuwa tayari kuchukua hatua za kujilinda na mali zao pale mvua hizo zitakapoanza.

Rais Samia amesisitiza kuwa kukabiliana na athari za mvua kubwa ni jukumu la pamoja, hivyo kila mmoja anatakiwa kutekeleza wajibu wake kwa wakati ili kupunguza uwezekano wa kutokea kwa maafa makubwa.



Na Janeth Raphael - MichuziTv

PWANI: Tanzania imeingia katika hatua mpya ya sekta ya nishati baada ya Kituo cha Kuzalisha Umeme cha Julius Nyerere (JNHPP) kuzinduliwa rasmi, huku mradi huo ukitarajiwa kuwa kichocheo muhimu cha shughuli za kiuchumi na kijamii nchini.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mradi huo leo, Jumamosi, Agosti 22, 2026, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema kukamilika kwa JNHPP ni matokeo ya msimamo wa Serikali wa kuwekeza katika miradi mikubwa yenye uwezo wa kubadilisha mazingira ya uzalishaji na upatikanaji wa umeme nchini.

Rais Samia amesema mradi huo una umuhimu wa kipekee kwa Tanzania kutokana na uwezo wake wa kuongeza uzalishaji wa umeme, akisisitiza kuwa Serikali haikuwa na sababu ya kuacha kuutekeleza kwa kuzingatia mchango wake katika maendeleo ya Taifa.

Rais Samia, amesema hatua ya sasa imefikiwa baada ya safari ndefu ya utekelezaji wa mradi huo, akirejea Desemba 22, 2022 aliposhuhudia hatua ya kufungwa kwa njia ya kuchepusha maji ya Mto Rufiji na kuanza kwa ujazaji wa bwawa.

Amesema awali ilitarajiwa bwawa hilo kujazwa ndani ya kipindi cha takribani miaka mitatu, lakini kutokana na kasi ya ujazaji maji, lilifikia kiwango kilichowezesha majaribio ya uzalishaji wa umeme ndani ya takribani mwaka mmoja na nusu.

Katika ziara yake wakati wa uzinduzi, Rais Samia alikagua miundombinu mbalimbali ya mradi huo, ikiwemo mitambo ya kuzalisha umeme, tuta kuu pamoja na kituo cha kupokea na kusafirisha umeme kwenda kwenye Gridi ya Taifa.

Amesema kuona miundombinu hiyo ikifanya kazi ni hatua kubwa na ya kujivunia kwa Tanzania, hasa kutokana na nafasi ya mradi huo katika kuimarisha uwezo wa nchi kukidhi mahitaji ya umeme yanayoongezeka.

JNHPP ina uwezo wa kuzalisha Megawati 2,115, kiwango kinachoongeza kwa kiasi kikubwa uwezo wa uzalishaji wa umeme nchini.

Ongezeko hilo linatarajiwa kutoa msukumo kwa sekta mbalimbali, ikiwemo viwanda, biashara, uwekezaji na huduma za kijamii, huku upatikanaji wa umeme wa uhakika ukiendelea kuwa msingi muhimu wa ukuaji wa uchumi.

Kwa kukamilika na kuzinduliwa kwa JNHPP, Tanzania sasa inaongeza uwezo wake wa kuzalisha umeme na kuweka mazingira bora zaidi ya kukabiliana na mahitaji ya nishati yanayoendelea kukua.


Na Belinda Joseph – Tanga

Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) imetajwa kuwa moja ya taasisi muhimu katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, kutokana na mchango wake katika kuwaandaa Watanzania wenye ujuzi unaohitajika katika uzalishaji na shughuli mbalimbali za kiuchumi.

Akizungumza na Michuzi TV Agosti 21, 2026, Meneja Mahusiano na Masoko wa VETA, Sitta Peter, amesema VETA itatumia nguzo tatu kwenye utekelezaji wa Dira ya Taifa ambazo ni uchumi imara, jumuishi na shindani, uwezo wa watu na maendeleo ya jamii, pamoja na uhifadhi wa mazingira na ustahimilivu wa mabadiliko ya tabianchi, yanahitaji nguvu kazi yenye ujuzi na umahiri.

Amesema katika kujenga uchumi imara na shindani, Tanzania inahitaji kuongeza tija katika uzalishaji, kuwekeza katika viwanda na kutekeleza miradi mbalimbali ya kiuchumi, ambayo yote yanahitaji wataalamu wenye uwezo wa kufanya kazi kwa ufanisi.

“Tunaposema tufanye uchumi wetu uwe imara na shindani, maana yake tunahitaji kuongeza tija kwenye uzalishaji, tunahitaji uwekezaji kwenye viwanda na tunahitaji utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kiuchumi, haya yote yanahitaji watu wenye ujuzi na umahiri."

Amesema vijana wanaopata mafunzo kupitia VETA wanaweza kunufaika na fursa zinazotokana na ukuaji wa sekta za uzalishaji, viwanda na miradi ya maendeleo kupitia ajira na kujiajiri, huku ujuzi ukiwawezesha pia kuongeza ufanisi katika shughuli kama kilimo na hivyo kuongeza uzalishaji na tija.

Amesema katika kutekeleza nguzo ya uhifadhi wa mazingira na ustahimilivu wa mabadiliko ya tabianchi, VETA tayari imepanda miti 130,800 katika vyuo vyake kote nchini, huku ikiendelea kutekeleza matumizi ya nishati safi ambapo vyuo 26 tayari vinatumia nishati hiyo, ikiwemo gesi na mkaa mbadala.

Ameongeza kuwa Chuo cha VETA Moshi kwasasa kinazalisha mkaa mbadala unaoweza kutumika kama nishati safi, huku kupitia Mradi wa Elimu na Stadi kwa Ajira zenye tija (ESPJ II) VETA ikipanga kuimarisha programu za usimamizi wa taka, matumizi sahihi ya rasilimali, utunzaji wa mazingira pamoja na afya na usalama mahali pa kazi.

Amesisitiza kuwa uwekezaji katika elimu na mafunzo ya ufundi stadi ni muhimu katika kujenga nguvu kazi yenye uwezo wa kuchochea tija, ajira na ukuaji wa uchumi, huku hatua za VETA katika mazingira na matumizi ya nishati safi zikiendelea kuunga mkono utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.



WAFANYAKAZI wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Kanda ya Mashariki wamefanya mazoezi ya kukimbia umbali wa takribani kilomita saba katika eneo la Coco Beach jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya kujiweka katika hali nzuri ya kiafya na utayari wa kutekeleza majukumu yao.

Akizungumza baada ya zoezi hilo leo Agosti 22, 2026 Jijini Dar es Salaam, Mhifadhi Mwandamizi wa TFS, Sunday Nachule, kwa niaba ya Kamanda wa Kanda ya Mashariki, amesema mazoezi hayo ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha askari wanakuwa timamu muda wote kwa ajili ya kutekeleza majukumu yao.

Amesema TFS itaendelea kuhamasisha watumishi wake kushiriki katika mazoezi ya mwili mara kwa mara ili kujenga afya na utayari wa kiutendaji.

Katika zoezi hilo, wanafamilia wa TFS wamepata pia fursa ya kufanya mazoezi pamoja na Mbunge wa Jimbo la Buchosa, Eric Shigongo, ambaye amewapongeza kwa juhudi hizo na kuwataka kuendelea na mazoezi.

Shigongo amesema misitu ni muhimu kwa uhai wa binadamu kutokana na mchango wake katika upatikanaji wa hewa safi na maji, hivyo wananchi wanapaswa kushirikiana na Serikali katika kuilinda.

Ametaja maeneo ya Buhindi na Lubondo yaliyopo katika Jimbo la Buchosa kuwa miongoni mwa maeneo yenye misitu inayosimamiwa na TFS, akisisitiza umuhimu wa wananchi kutunza rasilimali hiyo.

“Bila misitu hakuna uhai. Kwa hiyo nawaomba Watanzania waendelee kutunza misitu kwa sababu ni chanzo cha hewa na maji,” amesema Shigongo.

Aidha, ameipongeza TFS kwa kazi inayofanya katika kulinda na kuhifadhi misitu nchini, akieleza kuwa wananchi wanapaswa kuwa wadau wa uhifadhi kwa kuhakikisha rasilimali hiyo inalindwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.











Manyara Tanzanite Marathon 2026, mbio za hisani zenye lengo la kuchangisha fedha kwa ajili ya ujenzi na uwezeshaji wa wodi maalum ya kuwahudumia watoto njiti, zimefanyika leo katika Mji wa Babati, zikiwa na kaulimbiu “Hatua Moja, Okoa Maisha ya Mtoto Njiti.”

Mbio hizo za hisani zimeongozwa na Mgeni Rasmi kwa niaba ya Waziri Mkuu, Mhe. Mwigulu Nchemba, Naibu Spika wa Bunge, Mhe. Daniel Sillo, ambaye amempongeza Mkuu wa Mkoa wa Manyara kwa ubunifu wa kuanzisha Manyara Tanzanite Marathon, akieleza kuwa mbio hizo ni sehemu ya jitihada za kuchangia moja kwa moja katika kuokoa maisha ya watoto njiti.

Manyara Tanzanite Marathon 2026 inalenga kukusanya jumla ya shilingi bilioni 1.5, fedha zitakazotumika katika ujenzi na uwezeshaji wa wodi maalum kwa ajili ya kutoa huduma kwa watoto wanaozaliwa kabla ya wakati.

Mbio hizo zimewakutanisha wananchi na wanariadha kutoka maeneo mbalimbali, katika kuunga mkono juhudi za kuboresha huduma za afya na kuokoa maisha ya watoto njiti.

Mbio za Hisani za Manyara Tanzanite Marathon zimefanyika leo mkoani Manyara, zikihudhuriwa na watu mbalimbali kutoka maeneo tofauti ya nchi pamoja na viongozi mbalimbali, huku lengo kuu likiwa ni kuchangisha fedha kwa ajili ya kuokoa maisha ya watoto wachanga na watoto njiti.
Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Daniel Sillo, aliyemwakilisha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye alitarajiwa kuwa mgeni rasmi katika mbio hizo, amepongeza uongozi wa Mkoa wa Manyara kwa ubunifu wa kuanzisha mbio hizo zinazolenga kuchangisha fedha kwa ajili ya kuimarisha huduma za afya na kuokoa maisha ya watoto wachanga na watoto njiti.

Sillo amesema hatua hiyo ni mfano wa ubunifu unaopaswa kuigwa na maeneo mengine nchini, akisisitiza umuhimu wa kushirikisha jamii na wadau katika kusaidia kuboresha huduma za afya.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa TAMISEMI, Jafari Rajabu, amesema mbio hizo zimeleta tija kubwa katika juhudi za kuokoa maisha ya watoto, akiwataka wananchi na wadau kuendelea kuunga mkono jitihada zinazolenga kuboresha afya ya watoto.

Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, amewashukuru wadau wote walioshiriki na kuunga mkono maandalizi ya mbio hizo, akisema ushiriki wao umewezesha kufanikisha azma ya kuchangisha fedha kwa ajili ya watoto wanaohitaji huduma maalumu za afya.

Baadhi ya washiriki wa mbio hizo wamesema, pamoja na kushiriki kwa ajili ya mazoezi na kuimarisha afya zao, wameona umuhimu wa kuwa sehemu ya harakati za kuchangia maisha ya watoto wachanga na watoto njiti.

Wamesema ushiriki wao katika Manyara Tanzanite Marathon umewapa fursa ya kufanya mazoezi huku wakitoa mchango wa moja kwa moja katika kusaidia kuokoa maisha ya watoto, hivyo kuwataka wananchi wengine kuendelea kushiriki katika matukio yenye malengo ya kijamii na kiafya.




































 


Top News