Na: OWM – TAMISEMI, Lindi

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amesema hajaridhishwa na kasi ya utekelezaji wa miradi inayotekelezwa na Mkandarasi KIKIM Contractors Limited kwa kushirikiana na mbia wake AMACO Enterprises katika Manispaa ya Lindi.

Miradi hiyo inahusisha ujenzi wa barabara zenye urefu wa kilomita 5.3, Stendi ya Mabasi Mitwero, Soko Kuu la Matopeni na Ofisi ya Mradi, inayotekelezwa na Serikali kupitia Mradi wa Ustawishaji Miji Tanzania (TACTIC).

Prof. Shemdoe ameeleza kutoridhishwa kwake na kasi ya utekelezaji wa miradi hiyo Septemba 15, 2026, mara baada ya kutembelea na kukagua ujenzi wa Stendi ya Mabasi ya Mitwero na Soko Kuu la Matopeni, ambapo alibaini kuwa utekelezaji wake umefikia asilimia 23, huku ikiwa imesalia miezi mitano kabla ya muda wa kukamilisha na kukabidhi miradi hiyo.

Akizungumza baada ya kukagua miradi hiyo, Prof. Shemdoe amemtaka Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe. Adam Kighoma Malima, kuhakikisha suala la utekelezaji wa mikataba hiyo linashughulikiwa kwa mujibu wa masharti ya mikataba, ili kuharakisha utekelezaji na kuhakikisha miradi hiyo inakamilika kwa wakati.

“Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa, hawa wanaotukwamisha ni wakandarasi wazawa ambao usipowapa kazi wanalalamika. Hivyo, Mheshimiwa RC, hawa wana mikataba, shughulikia suala hili kwa mujibu wa mkataba, kwani wakandarasi hawa wanaonekana ni wababaishaji,” amesema Prof. Shemdoe.

Aidha, Prof. Shemdoe amemtaka Mkuu wa Mkoa wa Lindi kukutana na wakandarasi hao ili wampe mpango mkakati wa kukamilisha miradi hiyo haraka iwezekanavyo, na kuwasilisha kwake mpango kazi huo ifikapo Septemba 23, 2026.Vilevile, ameelekeza kuwa kila baada ya wiki mbili apatiwe mrejesho wa utekelezaji wa mpango huo, ili kufahamu hatua zinazochukuliwa na maendeleo ya miradi hiyo.

Akieleza chanzo cha kasi ndogo ya utekelezaji wa miradi hiyo, Mwakilishi wa Mhandisi Mshauri kutoka kampuni ya Interconsult Ltd, ambaye pia ni Mhandisi Mkazi, Mhandisi Rashidi Abdallah, amesema changamoto hiyo imetokana na mkandarasi kutokuwa amejipanga vyema kiutendaji, kutokuwa na rasilimaliwatu ya kutosha na kutumia vibaya fedha za awali alizolipwa kwa ajili ya utekelezaji wa mradi.

Naye mmoja wa Wakurugenzi wa kampuni zilizopewa kandarasi hizo, John Daniel, amekiri kuwa wamechelewa kutekeleza miradi hiyo kutokana na uzembe, huku akieleza kuwa wamejipanga kufanya kazi usiku na mchana baada ya kuzifanyia kazi changamoto zilizokuwa zikikwamisha utekelezaji.

Bw. Daniel ameomba kukutana na Mkuu wa Mkoa wa Lindi ili kuwasilisha mpango kazi wao, huku akimuomba Mkuu wa Mkoa kuwawekea malengo ya muda mfupi yatakayowawezesha kukamilisha kandarasi yao kwa wakati.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe. Adam Kighoma Malima, amesema atakutana na wakandarasi hao ili wamueleze mkakati wanaokuja nao wa kukamilisha miradi yote ndani ya miezi mitano iliyobaki.

Mhe. Malima amewataka wakandarasi hao, wakati wa kikao hicho, kuwa tayari kuridhia kutoa mkataba mdogo (sub-contract) kwa mkandarasi mwingine kutekeleza sehemu ya mradi endapo wataona hawana uwezo wa kuikamilisha kwa wakati.

Katika ziara yake ya Septemba 15, 2026, Prof. Shemdoe alitembelea na kukagua pia utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa Daraja la Ng’uni katika Kata ya Nanganga, ujenzi wa shule mpya ya msingi eneo la Shule ya Sekondari Kitandi, ujenzi wa Kituo cha Afya Chiola Nachingwea, pamoja na kufanya mkutano wa hadhara katika Kijiji cha Mtuha, Nachingwea DC.









RIYADH, SAUDI ARABIA:

Tanzania imesisitiza umuhimu wa kujenga na kutumia akili unde (Artificial Intelligence – AI) inayozingatia lugha, utamaduni, mazingira na mahitaji ya jamii, huku ikieleza dhamira ya kuimarisha uwezo wa ndani wa nchi katika teknolojia hiyo na kuongeza nafasi ya Kiswahili katika ulimwengu wa akili unde.

Msisitizo huo umetolewa katika Jukwaa la Nne la Kimataifa la UNESCO la Maadili ya Akili Unde linalofanyika mjini Riyadh, Saudi Arabia, ambapo Tanzania imeshiriki katika mjadala wa kimataifa kuhusu hatua za vitendo zinazoweza kuchukuliwa na nchi ili kuhakikisha maendeleo ya akili unde yanaenda sambamba na maadili, uwajibikaji, usalama na maendeleo jumuishi.

Katika mchango wake kwenye mjadala huo, mwakilishi wa Tanzania aliishukuru UNESCO na Serikali ya Saudi Arabia kwa kuandaa jukwaa hilo, akieleza kuwa majadiliano hayo yana umuhimu mkubwa katika kuzipa nchi nafasi ya kubadilishana uzoefu na kutafuta suluhisho la pamoja kuhusu fursa na changamoto zinazoletwa na maendeleo ya akili unde.


Aidha, Tanzania iliishukuru UNESCO kwa kuiunga mkono Serikali katika kutekeleza Mbinu ya Tathmini ya Utayari wa Akili Unde (Readiness Assessment Methodology – RAM) mwaka 2024, ambayo matokeo yake yalizinduliwa mwaka 2025.

Tathmini hiyo iliisaidia Tanzania kubaini maeneo mbalimbali yanayohitaji kuimarishwa ili kujenga mazingira wezeshi kwa maendeleo na matumizi salama, jumuishi na yenye maadili ya akili unde.

TANZANIA YASISITIZA KUJENGA UWEZO WA NDANI

Akieleza baadhi ya mapengo yaliyobainika, mwakilishi wa Tanzania alitaja umuhimu wa kuhakikisha lugha mbalimbali zinapata nafasi katika mifumo ya akili unde, akisisitiza kuwa nchi zinahitaji kujenga uwezo wa ndani ili teknolojia hiyo iweze kuakisi mazingira na mahitaji ya jamii zao.

Alieleza kuwa utegemezi mkubwa wa mifumo ya akili unde iliyotengenezwa nje unaweza kuibua changamoto zinazohusiana na uwakilishi wa tamaduni, usalama na umiliki wa data, pamoja na ulinganifu wa mifumo hiyo na sheria na maadili ya nchi husika.

Kwa msingi huo, Tanzania imeona umuhimu wa kuwekeza katika uwezo wa ndani wa kutengeneza na kutumia mifumo ya akili unde inayozingatia lugha na mazingira ya Tanzania, sambamba na kuimarisha miundombinu ya data na mifumo ya kitaifa ya usimamizi wa teknolojia hiyo.



Mwelekeo huo unaendana na hatua zinazochukuliwa na Serikali katika kuimarisha mageuzi ya kidijitali nchini. Serikali imetangaza mageuzi ya kidijitali kuwa miongoni mwa vipaumbele katika Bajeti ya mwaka 2026/2027, huku ikiendelea na maandalizi ya Mkakati wa Taifa wa Akili Unde.

KISWAHILI KUPATA NAFASI KATIKA MAPINDUZI YA AI

Moja ya hoja muhimu iliyowasilishwa na Tanzania Riyadh ni umuhimu wa kuendeleza mfumo mkubwa wa lugha (Large Language Model – LLM) wa Kiswahili, ili kuwezesha lugha hiyo kuwa sehemu muhimu ya maendeleo ya teknolojia za akili unde.

Tanzania imeeleza nia ya kushirikiana na wadau mbalimbali, wakiwemo UNESCO, katika kuendeleza mfumo huo, hatua inayolenga kuongeza uwezo wa teknolojia kuelewa na kutumia Kiswahili kwa ufasaha na kwa kuzingatia mazingira ya watumiaji wake.

Kiswahili kinachukua nafasi muhimu katika maisha ya Watanzania na ni miongoni mwa lugha zinazotumika na idadi kubwa ya watu barani Afrika. Kwa hiyo, uwekezaji katika teknolojia inayoweza kuelewa na kutumia Kiswahili una umuhimu katika kupanua ushiriki wa wananchi katika mapinduzi ya kidijitali.

Hatua hii pia inaendana na mwelekeo wa Serikali wa kuendeleza rasilimali na zana za lugha ya Kiswahili kwa ajili ya mifumo ya akili unde na uchakataji wa lugha asilia.

MAGEUZI YA KIDIJITALI KUELEKEA TANZANIA YA MAENDELEO

Mjadala wa Tanzania katika jukwaa hilo unaakisi mwelekeo mpana wa Serikali katika kutumia teknolojia za kisasa kama kichocheo cha maendeleo ya Taifa.

Katika hatua mbalimbali, Serikali imeendelea kuweka mazingira ya matumizi ya akili unde, ikiwemo kuimarisha sera na mifumo ya kidijitali, kulinda taarifa binafsi na kujenga uwezo wa rasilimali watu katika teknolojia zinazochipukia.

Mkakati wa Taifa wa Uchumi wa Kidijitali wa 2024–2034 pamoja na hatua zinazoendelea katika eneo la akili unde vinaweka msingi wa kutumia teknolojia za kisasa katika kuongeza ufanisi wa huduma, kukuza ubunifu na kuchochea shughuli za kiuchumi.

Kwa upande wa elimu, Serikali pia imeendelea kuweka msisitizo katika matumizi sahihi ya teknolojia mpya, ikiwemo akili unde, katika ufundishaji, ujifunzaji, utafiti na ujenzi wa uwezo wa walimu na wanafunzi.

TANZANIA NA AJENDA YA AI BARANI AFRIKA

Katika mjadala huo wa kimataifa, Tanzania imeendelea kuangazia pia nafasi ya Afrika katika mapinduzi ya akili unde, ikisisitiza umuhimu wa bara hilo kuongeza uwezo wake katika sayansi, teknolojia, utafiti, ubunifu na ujuzi wa kidijitali.

Kwa Tanzania, Afrika inapaswa kuwa zaidi ya mtumiaji wa teknolojia hiyo; inahitaji pia kujenga uwezo wa kuzalisha maarifa, data, mifumo na ubunifu unaozingatia mazingira ya Kiafrika.

Hii inamaanisha kuongeza uwekezaji katika wataalamu, taasisi za utafiti, miundombinu ya kidijitali na rasilimali za lugha za Kiafrika ili kuhakikisha maendeleo ya akili unde yanawanufaisha wananchi na kuchangia maendeleo ya bara.

UNESCO NA TANZANIA ZASHIRIKI KUJENGA AI YENYE MAADILI

Ushiriki wa Tanzania katika jukwaa la Riyadh unaendelea kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na UNESCO katika eneo la teknolojia zinazochipukia na matumizi yake yenye uwajibikaji.

Kupitia Tathmini ya Utayari wa Akili Unde, Tanzania imepata fursa ya kutathmini mazingira yake ya kitaifa na kubaini maeneo yanayohitaji kuimarishwa katika sera, mifumo ya kitaasisi, uwezo wa watu, miundombinu na matumizi ya teknolojia hiyo.

Kwa upande mwingine, ushiriki katika mijadala ya kimataifa kama ya Riyadh unaipa Tanzania nafasi ya kushirikisha uzoefu wake, kujifunza kutoka kwa nchi nyingine na kuendelea kujenga ushirikiano wa kimataifa katika eneo la akili unde.

Hatua hizi zinaendana na dhamira ya Serikali ya kutumia mageuzi ya kidijitali, sayansi, teknolojia na ubunifu kama nyenzo za kuongeza fursa za maendeleo na kujenga Tanzania inayokwenda sambamba na mabadiliko ya kiteknolojia duniani.

TANZANIA YAANGALIA MUSTAKABALI WA TEKNOLOJIA

Kwa ujumla, ujumbe wa Tanzania katika Jukwaa la Nne la Kimataifa la UNESCO la Maadili ya Akili Unde umeweka mkazo katika kujenga teknolojia inayozingatia watu, lugha na mazingira yao.

Kupitia mjadala huo, Tanzania imeendelea kuonyesha umuhimu wa kuunganisha maendeleo ya teknolojia na mahitaji ya jamii, huku ikisisitiza kuwa akili unde inapaswa kutumika kwa kuzingatia maadili, usalama, haki, utofauti wa lugha na tamaduni, pamoja na vipaumbele vya maendeleo ya Taifa.

Ushiriki huo unaendelea kuifanya Tanzania kuwa sehemu ya mjadala wa kimataifa kuhusu mustakabali wa akili unde, wakati Serikali ikiendelea kuchukua hatua za kujenga mazingira wezeshi ya mageuzi ya kidijitali na matumizi ya teknolojia kwa maendeleo ya Taifa.

Jukwaa la Nne la Kimataifa la UNESCO la Maadili ya Akili Unde linaendelea mjini Riyadh, Saudi Arabia, likiwakutanisha viongozi, wataalamu, watafiti, watunga sera na wadau kutoka sehemu mbalimbali duniani kujadili namna ya kuimarisha ushirikiano wa kimataifa na utawala wa akili unde unaozingatia maadili na uwajibikaji.

Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, amewasili mkoani Arusha leo Jumatano, Septemba 16, 2026, ambapo amepokelewa katika Uwanja wa Ndege wa Arusha na Mkuu wa Mkoa wa Arusha, CPA Amos Makalla, pamoja na viongozi wengine wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Serikali.

Dkt. Mwigulu yupo mkoani Arusha kwa ajili ya shughuli mbalimbali za kikazi, ikiwemo kufungua rasmi Kongamano la Kitaifa la Wanamipango, litakalofanyika kesho Alhamisi, Septemba 17, 2026, katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano Arusha (AICC).





Asasi za kiraia Zanzibar zitapata fursa ya kutumia huduma za kifedha za kidijitali kusimamia malipo, mishahara na fedha za taasisi kwa urahisi na uwazi zaidi, kufuatia makubaliano ya ushirikiano kati ya Mixx na Jukwaa la Asasi za Kiraia Zanzibar (ZANGOF).

Makubaliano hayo yatawezesha asasi zilizo chini ya ZANGOF kutumia huduma ya Mixx Business Suite kufanya malipo ya mishahara na wanufaika, pamoja na kusimamia miamala mingine ya taasisi kwa njia ya kidijitali. 

Asasi hizo pia zitaweza kupata huduma za mawasiliano na intaneti za Yas.Akizungumza katika hafla ya utiaji saini iliyofanyika leo Zanzibar, Mrajisi Mkuu wa Asasi za Kiraia Zanzibar, Ahmed Khalid Abdalla, alisema matumizi ya teknolojia yanaweza kusaidia asasi kuboresha usimamizi wa fedha na utoaji wa huduma kwa wananchi.

“Asasi za kiraia zinafanya kazi moja kwa moja na wananchi katika maeneo mbalimbali. Tunataka kuona teknolojia ikitumika kurahisisha kazi zao, kuongeza uwazi katika usimamizi wa fedha na hatimaye kuboresha huduma zinazotolewa kwa wananchi,” alisema Abdalla.

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa Mixx, Angelica Pesha, alisema ushirikiano huo utasaidia kupeleka huduma za kifedha za kidijitali karibu zaidi na asasi pamoja na jamii wanazozihudumia.

“Asasi hizi zinafanya kazi na wanawake, vijana, wajasiriamali na makundi mbalimbali katika jamii. Kupitia huduma zetu, tunataka kuwapa njia rahisi na salama zaidi za kusimamia fedha, kufanya malipo na kuweka akiba. 

Kwetu, ujumuishaji wa kifedha ni kuona huduma hizi zikimsaidia mwananchi kuboresha shughuli na maisha yake,” alisema Pesha.

Makubaliano hayo pia yanatoa fursa kwa vikundi vinavyofanya kazi na asasi za kiraia kutumia Kikoba cha Mixx, kinachowawezesha wanachama kuweka akiba, kuchangia, kununua na kuuza hisa pamoja na kukopeshana kwa njia ya kidijitali.

Mixx tayari inashirikiana na taasisi mbalimbali Zanzibar katika matumizi ya huduma za kidijitali, zikiwemo Idara ya Maendeleo ya Ushirika, ZARTSA, ZanBus na ZSTC, katika maeneo kama malipo ya wakulima, usafiri wa umma na huduma nyingine.

Makubaliano na ZANGOF yanatarajiwa kupanua matumizi ya huduma hizo kwa asasi za kiraia na vikundi vya kijamii Zanzibar.

 Afisa Mtendaji Mkuu wa Mixx Tanzania, Angelica Pesha (wa pili kulia), na Mratibu wa Jukwaa la Asasi za Kiraia Zanzibar (ZANGOF), Dkt. Mahfoudh Hassan Haji (katikati), wakionesha hati za makubaliano ya ushirikiano ambayo yatapanua upatikanaji wa huduma za kifedha za kidijitali kwa asasi za kiraia katika tukio lililofanyika leo visiwani humo.

 Wanaoshuhudia ni Mrajisi wa Asasi za Kiraia Zanzibar, Ahmed Khalid Abdalla (wa pili kushoto), Mkuu wa Yas – Zanzibar, Mohamed Waqid (kulia) na Mwenyekiti wa ZANGOF Ndugu Hassan Hamis Juma (kushoto). Kupitia ushirikiano huo, wanachama wa ZANGOF wataweza kutumia Mixx Business Suite kufanya malipo na miamala mingine ya kifedha kidijitali.

● Awasihi Watanzania kuchukua Vitambulisho vyao vya Uraia.

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali kupitia Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) itaanza kuchukua hatua za kuwasajili na kuwatambua watoto walio chini ya umri wa miaka 18, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha mfumo wa utambulisho wa Taifa.

Dkt. Mwigulu amesema hatua hiyo itamuwezesha kila Mtanzania kutambulika kuanzia hatua za mwanzo za maisha yake pamoja na kuondoa pengo lililokuwepo katika mfumo wa utambulisho kati ya mtoto anapozaliwa na anapofikisha umri wa miaka 18.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo, Jumatano, Septemba 16, 2026, wakati akiwa Mgeni Rasmi katika maadhimisho ya Siku ya Utambulisho Duniani, yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City, Dar es Salaam.

“Mfumo huu utasaidia kupunguza usumbufu wa kutumia nyaraka au vitambulisho vingi wakati wa kupata huduma mbalimbali, kwa kuwa taarifa muhimu za mwananchi zitaendelea kutambulika na kuhifadhiwa katika mfumo mkuu wa Taifa wa utambuzi” amesema.

Aidha, Dkt. Mwigulu amewataka Watanzania ambao tayari wamesajiliwa na vitambulisho vyao vya Taifa vimekamilika kwenda kuvichukua, akisisitiza kuwa utambulisho ni msingi muhimu wa maendeleo ya mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.

“Kitambulisho chenyewe kama nchi tumeingia gharama, tumeahirisha baadhi ya shughuli za maendeleo ili tutoe vitambulisho. Lakini tunapokuwa tumetoa kitambulisho, halafu mhusika haendi kuchukua, haya ni mambo ambayo yanakwamisha malengo mapana,” amesema.

Amesema kwa sasa NIDA imeboresha utaratibu wa kuwafahamisha wananchi pale vitambulisho vyao vinapokuwa tayari, ikiwemo kupitia ujumbe mfupi wa simu (SMS), hivyo hakuna sababu kwa wananchi waliokwishaandikishwa kuacha vitambulisho vyao kwa muda mrefu bila kuvichukua.

“Niendelee kusisitiza wananchi wote ambao wako tayari na vitambulisho vyao, basi waende kuvichukua. Lengo letu ni kuona kuwa hakuna Mtanzania anayeachwa nyuma katika kupata vitambulisho vya Taifa,” amesema.

Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu amesema Serikali imeendelea kufanya maboresho katika mfumo wa utambulisho wa Taifa ili kuhakikisha unakidhi mahitaji ya sasa ya kiteknolojia, usalama wa taarifa na utoaji wa huduma kwa wananchi.

“Serikali imeendelea kuboresha mfumo wa utambulisho ili kupunguza utegemezi wa vitambulisho vingi kwa huduma mbalimbali na kuelekea katika mfumo ambao taarifa muhimu za mwananchi zinapatikana kupitia mfumo mkuu wa Taifa wa utambuzi,” amesema.

Naye, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Patrobas Katambi, amesema NIDA imefanya mapitio ya jumla ya vitambulisho vilivyotolewa katika ofisi zake na vituo 10 vya usajili vilivyopo katika kila wilaya, bila kuhusisha vituo 156 vilivyotajwa awali.

Amesema hadi sasa jumla ya watu 27,520,835 wamesajiliwa, ambapo watu 23,515,667 wamekwishapatiwa Namba za Utambulisho wa Taifa. Aidha, vitambulisho 21,526,635 vimezalishwa, huku bado kukiwa na idadi ya vitambulisho ambavyo havijachukuliwa na wananchi waliostahili kuvipata.

Kwa Upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa NIDA, James Kaji, amesema jamii inapaswa kuacha dhana kwamba NIDA ni taasisi inayotoa kadi pekee, kwa kuwa utambulisho wa Taifa ni msingi wa upatikanaji wa huduma na utambulisho wa mwananchi katika maisha yake yote.

Amesema NIDA inaendelea kuboresha kitambulisho cha Taifa ili kiwe cha kidijitali na kiweze kuhusisha taarifa muhimu za huduma mbalimbali za kijamii, ikiwemo cheti cha kuzaliwa, bima ya afya, TIN, leseni ya udereva na taarifa nyingine muhimu, huku taarifa za kiafya kama kundi la damu zikitarajiwa kusaidia wakati wa dharura, kwa kuzingatia uthibitisho wa kitabibu.

Kanji amesema usajili wa watoto tangu wanapozaliwa ni muhimu kwa sababu utamwezesha kila mtoto kutambulika na kupata huduma za kijamii kwa urahisi katika hatua zote za maisha. Amesema zoezi hilo litaanza kwa majaribio katika wilaya za Kilolo, Lungu na Kusini Unguja, kabla ya kupanuliwa katika maeneo mengine nchini.








Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius Ndejembi amefanya mikutano miwili ya pande mbili (bilateral meetings) pembezoni mwa Mkutano Mkuu wa 70 wa Wakala wa Kimataifa wa Nguvu za Atomu (IAEA) Jijini Vienna, Austria, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Tanzania kuimarisha ushirikiano wa kimataifa katika maeneo mbalimbali ya maendeleo.

Katika mkutano wake na Mkurugenzi Mkuu wa IAEA, Bw. Rafael Mariano Grossi, mazungumzo yalijikita katika kuimarisha ushirikiano katika matumizi ya sayansi na teknolojia ya nyuklia kwa madhumuni ya amani na maendeleo, hususan matibabu ya saratani, kilimo na usalama wa chakula, lishe, maendeleo ya wataalamu pamoja na maandalizi ya Tanzania kuelekea matumizi ya nishati ya nyuklia kama nyongeza ya vyanzo vya uzalishaji umeme nchini siku zijazo.

Aidha, Makamu wa Rais amefanya mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa Vienna (UNOV) na Mkurugenzi Mtendaji wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Dawa za Kulevya na Uhalifu (UNODC), Dkt. Monica Juma. Mazungumzo yaliyolenga kuendeleza ushirikiano baina ya Tanzania na UNODC katika juhudi za kudhibiti dawa za kulevya.

Makamu wa Rais, Mhe. Ndejembi, yuko Jijini Vienna, Austria, akimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Mkutano Mkuu wa 70 wa Wakala wa Kimataifa wa Nguvu za Atomu (IAEA), unaowakutanisha Viongozi na Wawakilishi wa Nchi wanachama kujadili masuala mbalimbali yanayohusu matumizi salama na ya amani ya sayansi na teknolojia ya nyuklia.











Said Mwishehe,Michuzi TV

TANZANIA kupitia Benki Kuu (BoT) imepata tuzo tano za utambuzi zilitolewa na Jumuiya ya Huduma Jumuishi za Fedha( AFI) ikiwa ni sehemu ya kutambua hatua mbalimbali ilizochukua katika kuimarisha huduma jumuishi za kifedha.

Akizungumza leo Septemba 16,2026 jijini Dar es Salaam mbele ya waandishi wa habari kuhusu tuzo hizo Meneja wa Huduma Jumuishi za Kifedha wa Benki Kuu ya Tanzania, Nangi Massawe amesema AFI ilianzishwa mwaka 2009 .

Ameongeza kuwa AFI ina wanachama kutoka nchi 84 wakati taasisi wanachama zikifikia 90 huku lengo ni kuhakikisha wananchi wanapata na kutumia huduma rasmi za kifedha kwa usalama na kwa manufaa ya maendeleo yao na uchumi wa nchi.

Ameongeza mkutano wa AFI uliofanyika Septemba mosi hadi 4, mwaka huu nchini Guinea, Tanzania kupitia Benki Kuu imepata tuzo tatu kwa upande wa taasisi na tuzo mbili watu binafsi kutokana na utekelezaji wa mikakati ya huduma jumuishi za kifedha.

Amesema tuzo ya kwanza ni Maya Declaration Award, iliyotolewa kutokana na utekelezaji wa ahadi zilizowekwa na Tanzania, ambapo kati ya ahadi 13, nchi imetekeleza sita ikiwemo kuandaa na kutekeleza mkakati wa Huduma Jumuishi za Kifedha.

“Kwa sasa Tanzania inatekeleza mkakati wa tatu wa huduma jumuishi za kifedha uliowekwa mwaka 2023 na utatekelezwa kwa kipindi cha miaka mitano hadi mwaka 2028,” amesema Nangi

Pia amesema mafanikio mengine yaliyotambuliwa ni kuongezeka kwa kiwango cha ujumuishi wa kifedha kutoka asilimia 65 mwaka 2017 hadi asilimia 76 mwaka 2023, huku vipimo vya ndani vikionyesha kiwango hicho kimeendelea kukua na kufikia asilimia 80.

Nangi amesema idadi ya watu wazima wasio na huduma za kifedha nayo imepungua kutoka milioni 7.8 mwaka 2017 hadi milioni 6.4 mwaka 2022, wakati upatikanaji wa huduma za kifedha ndani ya umbali wa kilomita tano umeongezeka kutoka asilimia 86 hadi 89.

Pia amesema matumizi ya huduma za fedha kwa njia ya simu yameongezeka kutoka asilimia 60 hadi asilimia 72, huku pengo la huduma za kifedha kati ya wanawake na wanaume likipungua kutoka asilimia 10 mwaka 2017 hadi asilimia 3.2 mwaka 2022.

“Tanzania pia imeweka mfumo maalumu wa kumlinda mtumiaji wa huduma za kifedha kwa kuhakikisha malalamiko yanafikishwa sehemu sahihi na kufanyiwa kazi, pamoja na kuanzisha programu za elimu ya fedha kwa walio ndani na nje ya mfumo wa shule,”amesema Nangi.

Aidha amesema tuzo nyingine ilitokana na mafanikio ya sera za ujumuishi wa kifedha zinazozingatia wanawake, ikiwemo kuweka kipengele maalumu cha jinsia katika mkakati wa sasa, kubuni bidhaa zinazokidhi mahitaji ya wanawake, kupunguza vikwazo vya upatikanaji wa huduma na kuwezesha wanawake kupata huduma za mikopo na huduma nyingine rasmi za kifedha.

Kuhusu tuzo mbili za mtu binafsi amesema zikitolewa kwa watumishi wa Benki Kuu, akiwemo Dk. Khadija Kishimba na Nangi Massawe kwa kutambuliwa katika maeneo ya uongozi wa kiufundi na sera za huduma jumuishi za kifedha.

Awali Meneja Mifumo ya Malipo ya Taifa kutoka BoT, Mutashobye Mushumbusi ameeleza kuwa benki hiyo imeweka mwongozo wa gharama za huduma za kifedha kwa lengo la kuhakikisha wananchi wanapata huduma hizo kwa gharama nafuu.

“Mwongozo huo umeandaliwa kwa kushirikisha watoa huduma za kifedha na tayari umeanza kutumika,unasaidia kupunguza gharama za baadhi ya huduma,”amesema na kusisitiza BoT imeweka mkakati wa kuhakikisha taarifa za gharama za huduma za kifedha zinawekwa wazi kupitia tovuti pamoja na kuwataka watoa huduma kuonesha gharama hizo katika maeneo wanapotoa huduma.






Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira Tanzania (TRAMEPRO) limetoa salamu za pongezi kwa Baba Mtakatifu Leo XIV, katika kuadhimisha siku yake ya kuzaliwa, likimtakia afya njema, hekima, nguvu na neema katika kuendelea kutekeleza majukumu yake ya kichungaji.

Katika salamu hizo, TRAMEPRO limemshukuru Mwenyezi Mungu kwa zawadi ya maisha ya Baba Mtakatifu, huku likitambua uongozi wake wa hekima, unyenyekevu na dhamira ya kulitumikia Kanisa.

Shirika hilo pia limeeleza kuthamini ujumbe wa Baba Mtakatifu unaohimiza amani, umoja, huruma, heshima ya utu wa mwanadamu na mshikamano, sambamba na wito wa kulinda mazingira na dunia ambayo imekabidhiwa kwa binadamu.

TRAMEPRO limesema ujumbe huo una umuhimu katika kipindi ambacho dunia inakabiliwa na changamoto mbalimbali, ikiwemo mabadiliko ya tabianchi, uharibifu wa mazingira, umasikini na changamoto za afya.

Kwa mujibu wa shirika hilo, afya ya mwanadamu haiwezi kutenganishwa na afya ya mazingira, kwa kuwa maji safi, udongo salama, hewa safi, mimea ya dawa na mazingira bora ni sehemu muhimu ya maisha na ustawi wa jamii.

TRAMEPRO limemtakia Baba Mtakatifu Leo XIV maisha marefu yenye afya njema na utume wenye mafanikio, huku likimuombea aendelee kuwa sauti ya matumaini, amani na upendo kwa watu wote, wanyonge, wagonjwa na wanaohitaji faraja.

Katika salamu hizo, TRAMEPRO limesisitiza kuwa:

“Afya ya mwanadamu na afya ya mazingira ni urithi wa pamoja unaopaswa kulindwa kwa kizazi cha sasa na vizazi vijavyo.”

Salamu hizo zimetolewa na Boniventura F. Mwalongo, Katibu Mkuu wa Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira Tanzania (TRAMEPRO).TRAMEPRO limemalizia kwa kumtakia Baba Mtakatifu Leo XIV baraka na ulinzi wa Mungu, huku likiombea Kanisa, Tanzania, Afrika na dunia kwa ujumla.
Jane Mwakyoma ,Rukwa

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Charles Makongoro amewaomba wananchi na wadau mbalimbali kushiriki kikamilifu katika maandalizi ya kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2026, kinachotarajiwa kufanyika mkoani humo

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Makongoro amesema kilele hicho kitafanyika Jumatano, Oktoba 14, 2026, katika viwanja vya Nelson Mandela, Manispaa ya Sumbawanga.

Amesema shughuli za kilele hicho zitaambatana na matukio mbalimbali, ikiwemo maonesho ya fursa na shughuli za vijana, yatakayofanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi Ndua kuanzia Oktoba 8 hadi Oktoba 14, 2026.

Aidha amesema kutakuwa na Misa ya Kumbukizi ya miaka 27 ya kifo cha Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere itakayofanyika katika Kanisa Kuu Jimbo Katoliki Sumbawanga saa 12:00 asubuhi ya Oktoba 14, 2026, kabla ya kuendelea na sherehe za kilele cha Mwenge katika viwanja vya Nelson Mandela.

Aidha amewataka wananchi wa Rukwa kutumia fursa hiyo kujiinua kiuchumi kwa kufanya biashara mbalimbali, zikiwemo huduma za chakula, malazi, usafiri na usafirishaji kwa wageni watakaofika mkoani humo.

Amesema mkoa umejipanga kuhakikisha maandalizi ya kilele hicho yanafanyika kwa kushirikiana na Halmashauri zote nne,taasisi za umma, wadau na wananchi, huku akitoa wito kwa wananchi kushiriki katika kulinda amani na usalama wakati wa shughuli hizo .

Aidha Makongoro amesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa wananchi na wadau mbalimbali katika kuhakikisha kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2026 kinafanyika kwa mafanikio huku akiwataka wananchi kutumia tukio hilo kama fursa ya kukuza shughuli zao za kiuchumi na kudumisha amani na usalama wakati wote wa shughuli hizo.

Kilele hicho ni tukio muhimu la kihistoria kwa mkoa huo kuwa ni mara ya kwanza baada ya miaka 24 kwa mkoa huo kuwa mwenyeji wa kilele cha mbio za mwenge wa uhuru kitaifa ambapo uliwahi kuwashwa mkoani humo mwaka 1983 na 2002.




Na. Zawadi Msalla

Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB), ipo mbioni kuzindua mwongozo wa tathmini ya misingi ya utawala nchini.

Mwongozo huo umelenga kuangalia hali ya uzingatiwaji wa misingi ya utawala bora na kuweka mfumo unaoweza kutumika kupima namna taasisi za umma, binafsi na mifumo ya utawala inavyotekeleza misingi ya utawala bora.

Mwongozo huo pia imelenga kuwa nyenzo muhimu katika kubaini mafanikio yaliyofikiwa, changamoto zilizopo na maeneo yanayohitaji maboresho katika nyanja ya utawala bora.

Akizungumza katika kikao kazi cha kupitia rasimu hiyo kilichofanyika katika ukumbi wa Mkuu wa Mkoa Jijini Dodoma leo, Kaimu Katibu Mtendaji wa THBUB, Bi. Suzan Ndeona amesema kazi ya uandaaji wa nyaraka hiyo muhimu kwa nchi, ilianza rasmi mwaka 2023 kwa kuangalia vigezo mbalimbali na uhitaji wa nchi wa kuwepo mwongozo na nyenzo itakayotumika katika kufanya tathmini ya Utawala Bora nchini.

Bi. Suzan amesema mwongozo huo umeweka vigezo vyote muhimu vya upimaji wa uwepo wa utawala bora katika Taasisi. Aidha ameeleza mwongozo huo utaendelea kuboreshwa ili kuhakikisha unaenda sambamba na mabadiliko mbalimbali ya kimfumo yanayoendelea nchini kama vile upimaji wa Watumishi wa Umma (PEPMIS).

“Bado mwongozo huu ni rasimu, utakapokamilika utawekwa mezani kupata maoni ya taasisi za umma, binafsi, na mashirika mbalimbali ambayo yanahusika na masuala ya utawala bora”. Amesema Bi. Suzan.

Miongoni mwa misingi muhimu itakayoangaliwa na kufanyiwa tathimini ni pamoja na uwazi, uwajibikaji, usawa, utawala wa sheria, ushirikishwaji, ufanisi na tija, maridhiano, mwitikio na uadilifu.

Akieleza kuhusu misingi ya utawala bora, Bi. Suzan alisema misingi hiyo ina uhusiano wa moja kwa moja na jamii kwa kuwa utawala bora huonekana kupitia taasisi zinavyotoa huduma, kusikiliza wananchi, kutumia rasilimali na kutekeleza majukumu kwa mujibu wa sheria.

Naye Bi Hellen Siriwa kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) wakati wa kutoa wasilisho la rasimu hiyo, amesema NBS imeshirikiana kikamilifu na THBUB katika kuandaa nyenzo za kufanyia tathmini kwa kuangalia namna ambavyo nchi itafaidika na mwongozo huo ulioandaliwa. Aliongeza kuwa NBS itaendelea kushirikiana na THBUB katika kuhakikisha kuwa mwongozo huo unakamilika na kuweza kuzinduliwa rasmi Kitaifa.

Mwongozo huo utakuwa nyenzo ya kujenga utamaduni wa uwajibikaji katika taasisi za umma na binafsi kwa kutambua mapema maeneo yenye changamoto na kuchukua hatua za maboresho kabla ya kutokea kwa madhara.






Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Subira Mgalu amesema kuwa miongoni mwa masuala ambayo kamati hiyo itahakikisha inatekeleza ni pamoja na kufanikisha kuanzishwa kwa Bodi ya Usajili wa Wanajiosayansi Tanzania (Tanzania Geoscientists’ Registration Board).

Mgalu amesema hayo Jumatatu Septemba 14, 2026 Jijini Mwanza wakati akifungua Mkutano wa Mwaka wa Wajiolojia Tanzania ambapo alishiriki kama mgeni rasmi katika tukio hilo akiambatana na baadhi ya wajumbe wa kamati hiyo.

Katika hotuba yake ya ufunguzi, Mgalu amesema kuwa kukosekana kwa bodi ya kusimamia weledi wa kada ya wanajiosayansi kumesababisha uwepo wa vishoka wanaofanya kazi za kijiolojia bila ya kuwa na sifa stahiki hivyo kusababisha hasara kwa wawekezaji na Serikali kwa ujumla.

“Jambo hili limesababisha kutokukuwepo kwa mfumo thabiti wa kudhibiti maadili, viwango, taaluma, weledi na utaalamu wa wanajiosayansi walio katika utumishi wa umma na katika sekta binafsi nchini”

Kwa upande wao, Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini walioshiriki Mkutano wa Wajiolojia kwa mwaka 2026 akiwemo Mbunge wa Geita Vijijini, Joseph Musukuma na Mbunge wa Jimbo la Katoro, Kija Ntemi wamesema suala la uanzishwaji wa Bodi ni la msingi watahakikisha wanaibeba ajenda hii kikamilifu.


Kigoma, Septemba 16, 2026

Wadau mbalimbali wa sekta ya Uchukuzi na Usafirishaji wamekutana mjini Kigoma katika kikao cha siku moja kilichoandaliwa na Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), kwa lengo la kujadili fursa na changamoto zinazohusiana na usafirishaji wa mizigo na namna ya kuimarisha biashara katika ukanda wa Magharibi na Maziwa Makuu.

Kikao hicho kimehudhuriwa na wadau mbalimbali kutoka katika sekta ya Uchukuzi na Usafirishaji, ambapo Mgeni Rasmi, Mkuu wa Wilaya ya Kigoma, Dkt. Rashid Chuachua, kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, amesisitiza umuhimu wa ushirikiano miongoni mwa wadau katika kuimarisha ufanisi wa usafirishaji na kukuza biashara ya kikanda.

Kwa upande wa TPA, Naibu Mkurugenzi Mkuu, Mha. Dkt. Baraka Mdima, ameshiriki kikao hicho kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TPA, akiwakilisha uongozi wa Mamlaka katika majadiliano yaliyolenga kubaini maeneo ya kimkakati ya kuboresha huduma na kuongeza ufanisi wa usafirishaji kupitia Bandari ya Kigoma.

Majadiliano katika kikao hicho yamejikita katika kubaini changamoto zinazokwamisha mtiririko wa mizigo, zikiwemo vikwazo visivyo vya kiforodha, ucheleweshaji na gharama za usafirishaji, pamoja na kutafuta suluhu za pamoja zitakazoboresha mazingira ya biashara na kuongeza ushindani wa njia za usafirishaji.

Aidha, wadau wamejadili umuhimu wa kuimarisha matumizi ya Bandari ya Kigoma kama lango muhimu la biashara katika ukanda wa Maziwa Makuu, hususan kupitia Ushoroba wa Kati (Central Corridor) unaoiunganisha Tanzania na nchi jirani.

Kikao hicho pia kimekuwa fursa ya kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali, sekta binafsi na wadau wengine wa mnyororo wa usafirishaji katika kuboresha huduma, kupunguza muda na gharama za usafirishaji, na kuweka mazingira rafiki zaidi kwa biashara ya ndani na ya kikanda.

Kwa ujumla, kikao hicho kimeendelea kuonesha umuhimu wa majadiliano ya pamoja katika kutatua changamoto za usafirishaji na kutumia fursa zilizopo katika ukanda wa Magharibi, huku Bandari ya Kigoma ikiendelea kuwa sehemu muhimu ya kuunganisha biashara ya Tanzania na masoko ya nchi za Maziwa Makuu.












Top News