Taasisi ya Ramadhan Charity Programme 2026 imewataka Watanzania kutumia mwezi mtukufu wa Ramadhani kuwa wamoja, kusaidiana na kufanya kazi kwa pamoja katika kuwasaidia watu wenye uhitaji katika jamii.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Ramadhan Charity Programme 2026, Ahmed Misanga, wakati akikabidhi sadaka ya iftar katika kituo cha Jaamiul-Furouq, kilichopo wilayani Manyoni mkoani Singida.

Misanga amesema kuwa kutoa sadaka kunahitaji moyo wa kusaidia na si lazima mtu awe tajiri. Ameongeza kuwa watu wenye uwezo wajitokeze kushirikiana katika kuwasaidia wenye uhitaji, kwani wapo wengi hasa katika vituo vya kulea watoto yatima na watu wasiojiweza.

Aidha, Misanga amesisitiza kuwa kutoa sadaka na kutumia mali katika njia ya Allah ni miongoni mwa matendo mema na bora, kwani hufuta madhambi na makosa kama vile maji yanavyozima moto.

Katika hatua nyingine, amewahimiza vijana kusoma kwa bidii ili wawe watu wema katika jamii na baadaye waweze kusaidia wengine wenye uhitaji.

Kwa upande wake, Mwalimu Mkuu wa kituo hicho Nawawi Salimu, ameishukuru Taasisi ya Ramadhan Charity Programme 2026 kwa kuendelea kutoa sadaka ya iftar katika kituo hicho kwa mwaka wa tatu mfululizo.

Amesema msaada huo umekuwa na mchango mkubwa kwa wanafunzi wa kituo hicho, na amewahimiza wadau hao kuendelea na moyo huo wa kusaidia jamii, bila kuishia katika kituo hicho pekee bali kufikia pia vituo vingine vyenye uhitaji.

“Mimi pamoja na wanafunzi wangu hatuna cha kuwalipa, lakini tunaamini Mwenyezi Mungu ndiye atakayewalipa kwa wema huu mlioufanya,” amesema Nawawi.

Aidha, amewaomba wadau wengine kuiga mfano wa Ramadhan Charity Programme 2026 kwa kuwafikia walengwa na kutoa sadaka katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadhani, kwani bado kuna uhitaji mkubwa.

Ameongeza kuwa katika kituo hicho kuna zaidi ya watoto 100 wanaopata elimu ya dini na malezi ya mazingira, huku akisema milango ya msaada bado ipo wazi kwa yeyote mwenye nia ya kusaidia.




Dar es Salaam. Uganda na Tanzania zimekubaliana kuondoa vikwazo vyote vya biashara kati ya nchi hizo mbili ifikapo mwezi Juni mwaka huu, hatua inayolenga kupunguza gharama za kufanya biashara, kuimarisha biashara ya pande mbili na kukuza ushirikiano wa kiuchumi.

Ahadi hiyo ilitangazwa wakati wa chakula cha jioni rasmi kilichoandaliwa na Ubalozi wa Uganda nchini Tanzania jijini Dar es Salaam Alhamisi jioni, kuelekea Kikao cha Tano cha Tume ya Kudumu ya Pamoja kati ya Uganda na Tanzania (JPC).

Kikao hicho kimefanyika kuanzia Machi 11 hadi Machi 13, 2026 katika Julius Nyerere International Convention Centre, na kimewakutanisha maafisa wa serikali kutoka nchi zote mbili kujadili na kuimarisha ushirikiano katika sekta mbalimbali ikiwemo biashara, uwekezaji na ushirikiano wa kikanda.

Akizungumza katika hafla hiyo, Balozi wa Uganda nchini Tanzania, Fred Mwesigye, alisema nchi hizo mbili zina uhusiano wa kihistoria unaozidi urafiki wa kawaida na kufikia kiwango cha undugu wa karibu.

“Tungependa kuwaambia Watanzania na Waganda kwamba sisi si marafiki tu, bali ni ndugu. Kila tunachofanya tunakifanya kama ndugu—bila migogoro, bila vikwazo na bila changamoto zisizo za lazima,” alisema.

Kwa mujibu wa balozi huyo, lengo kuu la mazungumzo yanayoendelea kati ya serikali hizo mbili ni kuimarisha zaidi uhusiano wa kiuchumi na kuhakikisha wafanyabiashara wa pande zote wanafanya biashara bila vikwazo visivyo vya lazima.

“Tunapoelekea kwenye kikao cha tano cha JPC, tumekubaliana kuwa vikwazo vyote vilivyopo katika biashara vitaondolewa ifikapo mwezi Juni. Hii ina maana tunatarajia kuona nafaka zikiingia Uganda bila vizuizi, na wafanyabiashara wa Uganda wakifanya biashara Tanzania bila vikwazo,” alisema Balozi Mwesigye.

Alieleza kuwa baadhi ya tozo na gharama zinazohusiana na kodi zimekuwa miongoni mwa changamoto kubwa zinazoongeza gharama kwa wafanyabiashara kati ya nchi hizo mbili. Kuondolewa kwa vikwazo hivyo kutasaidia biashara kukua kwa kasi na kuimarisha ujumuishaji wa kiuchumi.

Balozi Mwesigye pia aliipongeza Tanzania kwa kuboresha miundombinu inayorahisisha biashara kati ya nchi hizo mbili.

Alitaja maendeleo ya barabara zinazounganisha Tanzania na Uganda, mipango ya kuufikisha Reli ya Kisasa (SGR) hadi Uganda pamoja na maboresho katika bandari zinazotumiwa na wafanyabiashara wa Uganda, ikiwemo Tanga, Mwanzana Dar es Salaam.

“Maboresho haya yatafanya usafirishaji wa bidhaa kati ya nchi zetu uwe rahisi zaidi. Mara tu gharama zilizobaki zitakaposhughulikiwa, biashara kati ya Uganda na Tanzania itakua kwa kasi zaidi,” alisema.

Balozi Mwesigye pia alizungumzia kile alichokiita kutokuwepo kwa uwiano katika uwekezaji kati ya nchi hizo mbili.

Alisema uwekezaji wa Watanzania nchini Uganda kwa sasa unazidi dola bilioni 2, huku uwekezaji wa Waganda nchini Tanzania ukiwa takribani dola milioni 200.

“Huo ni utofauti mkubwa. Lakini mara vikwazo vilivyosalia vitakapoondolewa, tunatarajia bidhaa za Uganda kama sukari kuingia Tanzania bila changamoto, huku bidhaa za Tanzania kama mchele zikifika kwa urahisi zaidi katika soko la Uganda,” aliongeza.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wa Uganda, Vincent Bagiire, aliwapongeza maafisa kutoka nchi zote mbili kwa mafanikio yaliyopatikana katika siku mbili za majadiliano kuelekea kikao cha JPC.

Alisema diplomasia ya kisasa inazidi kuelekeza nguvu katika masuala ya uchumi na biashara, huku majukwaa kama JPC yakisaidia kukuza biashara na uwekezaji kati ya nchi.

“Diplomasia ya sasa inalenga zaidi maslahi ya kiuchumi na kibiashara. Mifumo kama JPC ni nyenzo muhimu katika kutekeleza mtazamo huo na kusaidia kukuza uchumi wetu,” alisema.

Aidha alimpongeza Ubalozi wa Uganda jijini Dar es Salaam kwa juhudi zake katika kukuza ushirikiano wa kiuchumi kati ya nchi hizo mbili, ikiwemo mipango ya kuongeza mauzo ya bidhaa nje ya nchi.

Alitaja pia juhudi zinazoendelea za kuuza mabasi ya umeme yanayotengenezwa Uganda katika masoko ya kikanda ikiwemo Tanzania, akisema tayari kuna dalili kuwa mabasi hayo yanaweza kupata soko nchini Tanzania.

Waziri wa Nchi wa Mambo ya Nje wa Uganda anayeshughulikia Ushirikiano wa Kikanda, John Mulimba, alisema ushirikiano wa kikanda ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki unaendelea kuwa msingi muhimu wa kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi kati ya nchi wanachama.

Alibainisha kuwa mageuzi ya hivi karibuni ndani ya jumuiya hiyo yanatarajiwa kuboresha maamuzi na kuimarisha taasisi za kikanda.

“Tumekutana hapa kwa ajili ya JPC ili kuthibitisha upya dhamira yetu ya kutekeleza Itifaki ya Soko la Pamoja na Umoja wa Forodha. Mifumo hii tayari inatoa mwongozo wa masuala mengi tunayojadili,” alisema.

Alisisitiza kuwa hatua inayofuata ni kuhakikisha makubaliano yaliyofikiwa yanatekelezwa kwa vitendo.

“Lazima tuondoke hapa tukiwa na ratiba na majukumu yaliyo wazi ili wizara, idara na taasisi ziweze kutekeleza tuliyokubaliana badala ya kuweka nyaraka makabatini,” alisema.

Tume ya Kudumu ya Pamoja (JPC) ni jukwaa muhimu la ushirikiano wa pande mbili ambapo Tanzania na Uganda hupitia na kuimarisha ushirikiano katika sekta mbalimbali ikiwemo biashara, miundombinu, usalama na ujumuishwaji wa kikanda.

Na Mwandishi Wetu

WANAWAKE watatu wamebahatika kupata fursa ya kupandikiza mimba bure katika kituo cha kupandikiza mimba cha Kairuki Green IVF (KGIVF), Kilichoko Bunju A Mianzini jijini Dar es Salaam.

Walipata fursa hiyo jana jioni wakati wa droo iliyochezeshwa na mgeni rasmi Jokate Mwegelo wakati wa sherehe za siku ya wanawake zilizoandaliwa na Mtandao wa Elimu ya Afya Kairuki (KHEN) jijini Dar es Salaam .

Wanawake hao ni miongoni mwa wanawake zaidi ya 137 wa mikoa mbalimbali walioomba kupata fursa hiyo ya bure lakini katika mchujo uliofanyika walibahatika wanawake hao watatu pekee.

Kwa wastani gharama za kupandikiza mimba kwa Tanzania ni kati ya shilingi milioni 18 mpaka 20.

Mkurugenzi wa KGIVF, Dk Clementina Kairuki alisema waliopata fursa hiyo watahudumiwa bure kuanzia hatua za awali hadi kupandikiza mimba kama sehemu ya kituo hicho kusaidia jamii.

Alisema wameamua kutoa huduma hiyo bure kama sehemu ya kusherehekea siku ya mwanamke duniani kuwapa furaha ya kupata familia wanawake ambao wamekuwa wakitamani kupata familia lakini wanashindwa kutokana na kukosa pesa.

Alisema KGIVF iliona wanawake wengi wamekuwa wakijitokeza kutaka kupandikizwa mimba kwenye kituo hicho lakini asilimia 30 hawawezi kumudu gharama za huduma hiyo.

“Kuna watu wengi wanapata shida wanatukanwa kwenye familia wanaachika kwenye ndoa kwasababu hawajabahatika kupata watoto, tafiti zinaonyesha kuwa kila ndoa sita moja inachangamoto ya kupata watoto ndiyo maana tukaona tutoe fursa hii,” alisema

Alisema KGIVF imekuwa ikitoa elimu kwa jamii kuhusu ukubwa wa tatizo hilo na namna bora ya kupata suluhu ya kulitatua kwa kupandikiza mimba.

“Tumetambua kuwa kuna watanzania wengi wenye tatizo hili lakini hawana uwezo wa kuja KGIVF kupandikiza mimba kwasababu ya uwezo wa kifedha ndiyo maana tumechagua wanawake watatu tuwape huduma hii bure kama sehemu ya kutoa elimu kwa jamii,” alisema

Mgeni rasmi kwenye hafla hiyo, Jokate Mwegelo alisema Mtandao wa Elimu ya Afya Kairuki (KHEN) ni mfano wa kuigwa ukanda wa Afrika Mashariki na Kati kutokana na mambo makubwa waliyofanya.

Alisema KHEN imefanya mambo makubwa ikiwemo kuanzisha Kituo cha kupandikiza mimba KGIVF, Kairuki Hospitali, Kiwanda cha kutengeneza dawa kilichoko Kibaha mkoani Pwani, Chuo Kikuu Kairuki na Kampasi ya chuo hicho iliyoko Boko.

“Mimi ni mdau mkubwa sana wa Kairuki, nimekuwa nikiwasemea sana na leo naomba nijirasimishe kuwa balozi wa Kairuki, nitawasemea vizuri popote nitakapokuwa kwasababu nyinyi mmeonyesha mfano wa kuigwa kwenye kusaidia jamii yetu,” alisema Jokate Mwegelo.

“Mimi nitakuwa balozi wa viwango kwasababu nimeona Kairuki ni taasisi ya viwango vya juu sana, siongei haya kumfurahisha mtu hapa nasema hili kutoka kwenye sakafu ya moyo wangu, katika taasisi zilizoasisiwa na watanzania wenzetu, Kairuki ni taasisi ya mfano Afrika Mashariki na Kati kwasababu imesimama na haitetereki,” alisema

“Wako watu walianzisha biashara hata miaka mitatu haijafika zikafa, lakini leo hii ukizungumzia Kairuki unazungumzia Hospitali, unazungumzia Kairuki Green IVF, unazungumzia kiwanda cha dawa Kibaha, chuo cha Kairuki ambacho kinawanafunzi zaidi ya 2,000 nani kama Kairuki,” alisema




















📌 Umeme umewashwa kwa mara ya kwanza katika vitongoji viwili

📌 Zaidi ya Shilingi bilioni 60 zatumika kusambaza umeme kwenye vitongoji vya mkoa wa Shinyanga


Kahama, Shinyanga📍

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imeridhishwa na namna fedha za Bajeti ya Mwaka 2025/2026 zilizoidhinishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zinavyotumika katika utekelezaji wa Miradi ya kusambaza umeme kwenye vitongoji kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA).

Akizungumza wakati wa ziara ya Kamati pamoja na zoezi la kuwasha umeme kwa mara ya kwanza katika kitongoji cha Mine, kata ya Mwakata, Jimbo la Msalala na kitongoji cha Mjimwema katika Jimbo la Kahama wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Subira Mgalu, amesema ziara ya kamati imelenga kukagua na kujionea utekelezaji wa Miradi ili kuhakikisha fedha zilizotengwa na Bunge zinatumika kwa ufanisi.

“Tumepewa dhamana na Bunge kuhakikisha fedha zilizotengwa zinatekeleza kusudi lililokusudiwa. Bunge lilitenga bajeti ya shilingi bilioni 400 kwa mwaka wa fedha 2025/2026 kwa ajili ya miradi ya kufikisha umeme vitongojini, na tumekuja kuona thamani ya fedha hizo kama imetumika ipasavyo. Kwa kweli tumeridhishwa na kazi inayofanywa na REA,” amesema Mhe. Mgalu.

Ameongeza kuwa utekelezaji wa miradi hiyo unaonesha mafanikio makubwa ya Serikali ya Awamu ya Sita ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inayoongozwa na  Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuhakikisha wananchi wa vijijini wanapata huduma ya umeme.

Naye Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, amesema ukaguzi wa miradi unaofanywa na Kamati ya Bunge ni sehemu muhimu ya utekelezaji wa Katiba, inayolenga kuhakikisha Bunge linasimamia ipasavyo matumizi ya fedha za umma katika miradi ya maendeleo.

Makamba amesema katika bajeti ya Wizara ya Nishati, ilipanga kuwa kila jimbo nchini litapatiwa vitongoji 15 vitakavyofikishiwa huduma ya umeme ili kuongeza kasi ya maendeleo kwa Wananchi.

Amesema Miradi hiyo inaendelea kubadilisha maisha ya Wananchi kwa kuchochea shughuli za kiuchumi pamoja na kuboresha huduma za kijamii na kuongeza fursa za maendeleo katika maeneo ya vijijini.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Umeme Vijijini kutoka REA, Mhandisi Jones Olotu aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa taasisi hiyo, amesema mkoa wa Shinyanga una jumla ya vitongoji 2,704 ambapo kati ya hivyo vitongoji 1,180 tayari vimefikishiwa huduma ya umeme.

Amesema vitongoji 582 vipo katika Mradi wa HEP II (B); Mradi uliosainiwa Januari mwaka huu ambao unatarajiwa kukamilika ndani ya kipindi cha miaka mitatu.

“Kuanzia mwaka wa fedha 2024/2025 hadi sasa REA imeidhinisha zaidi ya shilingi bilioni 61 kwa ajili ya kufikisha umeme katika vitongoji mbalimbali vya mkoa wa Shinyanga,” amesema Mhandisi, Olotu.

Aidha ameahidi kuwa REA itaendelea kutekeleza maelekezo ya Serikali na Bunge kuhakikisha ifikapo mwaka 2030 vitongoji vyote nchini vinafikiwa na huduma ya umeme.









Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Miundombinu ikipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania (TRC) Mhandisi Mhandisi Machibya Shiwa wakati Kamati hiyo ilipotembelea na kukagua mradi wa uundaji wa vichwa vya Treni za MGR  unaoendelea katika Karakana ya Pugu jijini Dar es Salaam.

Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Miundombinu ikwa katika moja ya kichwa katika kilichoundwa  wakati walipotembelea na kukagua mradi wa uundaji wa vichwa vya Treni za MGR  unaoendelea katika Karakana ya Pugu jijini Dar es Salaam.
Kichwa cha Treni za MGR kilichoundwa katika Karakana ya Pugu jijini Dar es Salaam.

*Tanzania yawa nchi ya kwanza katika ukanda wa Afrika Mashariki

Na Mwandishi Wetu 

Kamati ya Bunge ya  Kudumu ya Miundombinu, imelitolea wito Shirika la Reli Tanzania (TRC) kuendelea kuwajengea uwezo vijana wa Kitanzania wanaounda na kukarabati vichwa vya treni za MGR, kwa kuwapa mafunzo thabiti ndani na nje ya nchi ili kuongeza maarifa, stadi na ubunifu katika utendaji wao kazi hiyo  .

Hayo ameyasema  Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya  Kudumu ya Miundombinu  Selemani Kakoso,  wakati wa ziara ya kamati hiyo iliyolenga kukagua mradi wa uundaji wa vichwa vya treni za MGR, unaoendelea katika karakana ya Pugu, Jijini Dar es Salaam. 

Kakoso kwa niaba ya kamati hiyo, ameitaka TRC kuhakikisha  inawapa fursa na kuwapeleka vijana hao wenye ujuzi nje ya nchi kujifunza  na kuchota utalaamu zaidi ili kuongeza ufanisi katika utendaji wao, aidha alitoa rai kwa TRC  kuwapa k kipaumbele katika suala la ajira  ili waendelee kulitumikia shirika na nchi kwa uaminifu.

Aidha Kakoso, alisema kamati inaipongeza kwa dhati  TRC na Mkurugenzi wake Mkuu Mhandisi Machibya Shiwa, ambapo  kwa mara ya kwanza katika historia, Tanzania  imefanikiwa kufanya hivyo kufuatia ucheleweshwaji wa vipuri kimkataba kutoka kwa wazabuni wa vipuri wa SMH Kutokana vita kati ya Ukraine na Urusi, hivyo TRC ilifanya maamuzi ya kusafirisha vichwa viwili vilivyokamilika na kuundwa nchini Malaysia na kusafirisha vipuri kutoka kw wazabuni kuja nchini na kuanzaz uundwaji wa vichwa sita vilivyobaki katika karakana ya Pugu.

Kakoso, ameongeza kusema kuwa uamuzi wa TRC kuunda  vichwa vya treni hapa nchini  umepunguza gharama kubwa ambayo serikali ingetumia kuagiza vichwa hivyo na pia imewezesha vijana wengi wa Kitanzania wenye ujuzi kuajiriwa aidha Mhe. Kakoso amewaasa watumishi wa Shirika la Reli Tanzania kuwa wazalendo katika kulitumikia Shirika na kutunza rasilimali zilizopo na kuepuka vitendo vya hujuma kwa  shirika.

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri wa Wizara ya Uchukuzi Mhe.David Kihenzile, ameendelea kuipongeza Serikali kupitia TRC kwa kukuza sekta ya uchukuzi kwa kuendelea kujenga  miundombinu bora na yenye ufanisi na kununua vitendea kazi ikiwemo vichwa na behewa.

"Nampongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuboresha sekta ya uchukuzi , serikali imeendelea na ujenzi wa reli ya kisasa zaidi ya kilomita 2290 na sasa inanunua vitendea ili kuboresha sekta hii." alikazia  Mhe.Kihenzile.

Awali Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania Mhandisi Machibya Shiwa, Pamoja na masuala mengine, aliiambia kamati hiyo ya kudumu ya Bunge ya Miundombinu juu ya manufaa ya mradi wa uundaji wa vichwa vya treni za MGR Daraja la 91XX katika karakana ya Pugu, ni Pamoja na fursa za ajira amabpo jumla ya vijana 34 ambao hawakuwa wameajiriwa sasa wameajiriwa kupitia mradi huo. Aidha Mhandisi Shiwa, alisema, “kupitia mradi huo baadhi ya Watanzania, wamepata kuuza bidhaa zinazotumika katika uundaji wa vichwa hivyo nao ni kama wenye mashine za kuchinga vipuri, wauzaji wa vifaa ujenzi, bolt na nati, wauzaji vifaa vya umeme, mabomba, wauzaji vilainishi, bidhaa za mpira nk’’, alimalizia Mkurugenzi mkuu huyo wa TRC.






Matukio mbalimbali katika picha ya Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Miundombinu   ilipotembelea na kukagua mradi wa uundaji wa vichwa vya Treni za MGR  unaoendelea katika Karakana ya Pugu jijini Dar es Salaam.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM), Dkt. Maulid J. Maulid, amefungua kikao kazi cha Chama cha Kulinda na Kutetea Haki za Walimu (CHAKUHAWATA) kinachofanyika jijini Dodoma, akisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya wadau mbalimbali wa sekta ya elimu ili kuimarisha uongozi, utawala bora na udhibiti wa ubora wa elimu nchini.

Akizungumza katika hafla ya ufunguzi wa kikao hicho, Dkt. Maulid amesema ADEM imekuwa ikifanya kazi kwa karibu na jumuiya mbalimbali za elimu zikiwemo TAHOSSA, TAPSHA na REDEOA pamoja na mashirika ya kitaifa na kimataifa, kwa lengo la kuunganisha nguvu katika kufanikisha malengo ya kitaifa ya maendeleo ya elimu.

Amesema mwaliko wa kushiriki katika kikao hicho muhimu cha wadau wa sekta ya elimu umefungua ukurasa mpya wa ushirikiano kati ya ADEM na CHAKUHAWATA, kwani hapo awali taasisi hizo hazikuwa na ushirikiano wa karibu katika shughuli zao.

“Taasis yetu itaitumia fursa hii na jukwaa hili muhimu kuhakikisha tunafanya kazi kwa karibu kuwajengea uwezo walimu na viongozi wa elimu nchini,” amesema Dkt. Maulid.

Aidha, ameipongeza CHAKUHAWATA kwa juhudi zake za kutekeleza majukumu yake na kwa namna inavyowasaidia wanachama wanaokumbwa na changamoto mbalimbali ikiwemo masuala ya ajira, majanga na ustawi wa walimu.

Dkt. Maulid amesema juhudi hizo zimechangia kukua kwa chama hicho kutoka wanachama 182 wakati wa kuanzishwa kwake mwaka 2015 hadi kufikia wanachama 49,750 kwa sasa.

Amesisitiza pia umuhimu wa kuimarisha mawasiliano kati ya chama hicho na taasisi au wizara zinazowasimamia waajiri wa wanachama wao ili kujenga uelewa wa pamoja na kutatua changamoto zinazojitokeza kwa njia za kisheria na maelewano.

Katika hatua nyingine, amewahimiza viongozi wa CHAKUHAWATA kusimamia matumizi sahihi ya rasilimali za wanachama na kuimarisha ushiriki wa wanachama katika vikao vya chama ili kutoa mawazo yatakayosaidia kukijenga chama kwa mujibu wa katiba yake.

















Top News