Na Mwandishi Wetu 
CHUO Kikuu cha Dodoma (UDOM), kupitia Mradi wa SAFARI unaotekelezwa kwa ushirikiano na Liverpool School of Tropical Medicine, kimebuni teknolojia ya matumizi ya akili Unde (Artificial Intelligence) inayolenga kusogeza huduma za uchunguzi wa ujauzito (Ultrasound) karibu na wajawazito wanaoishi katika maeneo yenye upungufu wa wataalamu wa afya.

Akizungumza katika Maonesho ya Nanenane yanayoendelea viwanja vya Nzuguni jijini Dodoma, mtafiti wa mradi huo, Hamim Rushoke, amesema mfumo huo unatumia kifaa chenye Kumputa na probe maalumu inayowekwa tumboni kwa mjamzito, ambapo akili unde huchambua taarifa na kutoa majibu ndani ya dakika moja bila kuhitaji mtaalamu wa Ultrasound.

Amesema kifaa hicho kina uwezo wa kubaini umri wa ujauzito, hali ya uhai wa mtoto, mapigo ya moyo, idadi ya watoto waliopo tumboni pamoja na mkao wa mtoto ikiwa ametanguliza kichwa au miguu, kisha kutoa ripoti ambayo inaweza kusomwa na mhudumu yeyote wa afya.

"Teknolojia hii imebuniwa kuondoa changamoto ya ukosefu wa wataalamu wa ultrasound katika zahanati na vituo vya afya. Hata nesi au mkunga akipewa mafunzo ya siku mbili hadi tatu anaweza kuitumia kwa urahisi na kupata majibu sahihi kwa muda mfupi," amesema Rushoke. Ameeleza kuwa lengo kuu la mradi huo ni kuhakikisha wajawazito wa maeneo ya vijijini wanapata huduma za uchunguzi mapema, akibainisha kuwa wanawake wengi hufikia hatua ya kujifungua bila kufanyiwa hata kipimo kimoja cha ultrasound, jambo linaloweza kuhatarisha afya ya mama na mtoto. Kwa mujibu wa Rushoke, kwa sasa mradi huo uko katika hatua ya upembuzi yakinifu ukifanyika chini ya usimamizi wa Wizara ya Afya na Ofisi ya Rais-TAMISEMI, huku ukishirikisha viongozi wa afya, wajawazito na jamii ili kupima namna ambavyo ubunifu huo unapokelewa kabla ya kuidhinishwa kutumika nchini. "Tumepata ushirikiano mkubwa kutoka Wizara ya Afya, TAMISEMI, viongozi wa afya ngazi zote, wahudumu wa afya pamoja na wanawake wajawazito. Dalili zinaonyesha kuwa jamii ipo tayari kuupokea mfumo huu mara baada ya kukamilika kwa utafiti," amesema.

Aidha, amesema mradi huo umezingatia matumizi ya vifaa vya gharama nafuu ikilinganishwa na mashine za kawaida za ultrasound ambazo zinaweza kugharimu zaidi ya Sh milioni 80, wakati mfumo huo unahitaji tablet na probe zenye gharama zisizozidi Sh milioni tano kwa kifaa kizima.

Rushoke amesema mradi huo utaacha vifaa 32 katika zahanati na vituo vya afya 32 vya mkoa wa Dodoma vilivyotumika katika utafiti ili viendelee kutoa huduma bure kwa wananchi, huku akieleza kuwa hatua inayofuata ni Serikali kupanga bajeti ya kusambaza teknolojia hiyo katika maeneo mengine nchin



Na Mwandishi Wetu, Dodoma
MSULUHISHI wa Migogoro ya Bima (TIO) amewataka wakulima waliokata bima za kilimo kupitia benki au mawakala wa bima, kutumia Ofisi ya Msuluhishi wa Migogoro ya Bima pale wanapokumbana na migogoro ya fidia ili kupata haki zao badala ya kukimbilia mahakamani.

Akizungumza katika Maonesho ya Kilimo ya Kimataifa Nanenane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samwel Malecela jijini Dodoma, Msuluhishi Mkuu wa TIO Aloyce Mbunito, alisema ofisi hiyo iliyoanzishwa kwa mujibu wa Sheria Sura ya 394 ina jukumu la kutatua migogoro ya bima kwa njia mbadala ya mahakama.

Alisema ofisi hiyo pia inalenga kulinda watumiaji wa huduma za bima na kuongeza imani ya wananchi katika sekta hiyo.

Mbunito alisema migogoro inayopokelewa mara nyingi inahusisha kukataliwa kwa madai ya fidia, kulipwa fidia isiyolingana na hasara halisi, kucheleweshwa kwa majibu ya madai pamoja na kutokuelewana kuhusu tafsiri ya mikataba ya bima.

Alisema tangu ofisi hiyo ianze kazi mwaka 2025, imefanikiwa kutatua zaidi ya migogoro 2,015, jambo alilosema linaonyesha kuwa wananchi wameanza kutambua umuhimu wa kuitumia kupata haki zao wanapokumbana na changamoto katika huduma za bima.

Aidha, Mbunito alisema katika maonesho hayo wamepokea viongozi wa vyama vya ushirika vya wakulima kutoka mkoani Mara, waliowasilisha changamoto zinazowakabili wakulima wa tumbaku waliopata hasara kutokana na mvua ya mawe, licha ya kuwa walikuwa wamekata bima kupitia benki.

Kwa mujibu wa Mbunito, changamoto kubwa iliyobainika ni baadhi ya wakulima kutofahamu kampuni za bima zilizowahudumia kwa kuwa walikata bima kupitia benki zilizokuwa mawakala wa kampuni hizo.

Alisema pia baadhi ya wakulima hawana mikataba ya bima, ambayo ni nyaraka muhimu katika kufuatilia madai ya fidia pale wanapopata hasara.

Naye Mwenyekiti wa Chama Kikuu cha Ushirika Mara (WAMACU), Momanyi Range, alisema elimu waliyoipata katika banda la Ofisi ya Msuluhishi wa Migogoro ya Bima imewafungua macho kuhusu umuhimu wa kuwa na mikataba ya bima pamoja na kuhifadhi ushahidi wa majanga.

Alisema ushahidi huo unaweza kujumuisha picha za mazao yaliyoharibiwa na majanga, hatua ambayo inaweza kusaidia kurahisisha mchakato wa madai ya fidia.

Range alisema chama hicho sasa kitawaongoza wakulima walioathiriwa kukusanya malalamiko yao, kupata mikataba ya bima kutoka benki husika na kuyawasilisha katika Ofisi ya Msuluhishi wa Migogoro ya Bima ili kuhakikisha wanapata haki zao.

Alisema hatua hiyo itasaidia kuwawezesha wakulima kukabiliana na hasara zinazotokana na majanga na kuendelea na shughuli za uzalishaji bila kuathiriwa zaidi na athari za majanga hayo.


Farida Mangube, Morogoro

Tanzania imepiga hatua katika kuelekea kujitosheleza kwa sukari kufuatia kuanza rasmi kwa uzalishaji katika Kiwanda kipya cha Kisasa cha Sukari Kilombero K4 kilichopo mkoani Morogoro, ambacho kimegharimu zaidi ya shilingi bilioni 700.

Uwekezaji huo unatarajiwa kuongeza uzalishaji wa sukari nchini, kupunguza utegemezi wa uagizaji kutoka nje na kuchochea ukuaji wa uchumi.

Akizungumza katika maonesho ya nanenane Kanda ya Mashariki Mkurugenzi wa Biashara wa Kiwanda cha Sukari Kilombero, Fimbo Butallah, amesema kuanza kwa uzalishaji katika kiwanda hicho kutasaidia kuziba pengo la upungufu wa sukari nchini na kuongeza upatikanaji wa bidhaa hiyo kwa wananchi.

Butallah amesema pia kiwanda hicho kimezingatia tofauti za vipato vya Watanzania kwa kuzalisha sukari katika ujazo wa aina mbalimbali, hatua itakayowezesha wananchi kupata bidhaa hiyo kulingana na uwezo wao wa kifedha.

Kwa upande wake, Meneja wa Ufuatiliaji na Uthibitishaji kutoka Bodi ya Sukari Tanzania, Bahati Hakimu, amesema kukamilika kwa Kiwanda cha Kilombero K4 ni hatua muhimu katika kuongeza uzalishaji wa sukari nchini, huku pia kikitarajiwa kuongeza ajira kwa wakulima wa miwa na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika Bonde la Kilombero.





Na Janeth Raphael -MichuziTv 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametoa wito kwa viongozi wa nchi za Afrika kuharakisha utekelezaji wa miradi ya miundombinu, akisisitiza kuwa maendeleo ya Bara hilo hayatapimwa kwa mipango na sera pekee, bali kwa matokeo yanayoonekana katika maisha ya wananchi.

Rais Samia ameyasema hayo leo jijini Dar es Salaam wakati akifungua Jukwaa la Miundombinu Afrika pamoja na Mkutano Mkuu wa Wanahisa wa Africa50, ambapo alieleza kuwa uwekezaji katika miundombinu ni nguzo muhimu ya kukuza uchumi, kuongeza ushindani wa Afrika, kuvutia wawekezaji na kuimarisha biashara ndani ya bara.

Amesema wananchi wanahitaji kuona matokeo kupitia ujenzi wa barabara bora, reli za kisasa, bandari zenye ufanisi, nishati ya uhakika, maendeleo ya teknolojia pamoja na kuongezeka kwa fursa za ajira.

Akizungumzia hatua zinazochukuliwa na Tanzania, Rais Samia alisema Serikali inaendelea kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kujenga uchumi wa viwanda, jumuishi na unaotegemea ubunifu, ujuzi pamoja na miundombinu ya kisasa.

Amebainisha kuwa Serikali imeendelea kuwekeza katika kuboresha Bandari ya Dar es Salaam, Reli ya Kisasa (SGR), barabara, madaraja na korido za kimkakati ili kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha biashara na usafirishaji katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika.

Rais Samia amesema uwekezaji huo hauwanufaishi Watanzania pekee, bali pia unahudumia nchi jirani zisizo na bandari, zikiwemo Burundi, Rwanda, Uganda, Zambia, Malawi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), hivyo kuimarisha nafasi ya Tanzania kama lango muhimu la biashara na uwekezaji barani Afrika.

Aidha, amesisitiza kuwa Afrika inapaswa kuongeza thamani ya rasilimali zake badala ya kuendelea kusafirisha malighafi, hatua ambayo itaongeza ajira, ujuzi na uwezo wa uzalishaji ndani ya bara.

Katika sekta ya nishati, Rais Samia alieleza kuwa gesi asilia ina nafasi kubwa katika kuimarisha usalama wa nishati, kusaidia ukuaji wa viwanda na kuchochea maendeleo ya uchumi wa Tanzania pamoja na nchi nyingine za Afrika.

Kwa upande wake, Naibu Rais wa Kenya, Prof. Kithure Kindiki, alisema mafanikio ya miradi mikubwa ya miundombinu yanategemea uongozi madhubuti wa kisiasa, sera thabiti na mipango ya muda mrefu.

Prof. Kindiki pia amezitaka nchi za Afrika kuwekeza katika kujenga uwezo wa wataalamu wa ndani, kutumia mifumo bunifu ya kugharamia miradi na kuhakikisha wananchi wanashirikishwa kikamilifu ili wanufaike na maendeleo yanayotekelezwa.

Naye Mwenyekiti wa Africa50 ambaye pia ni Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Dkt. Sidi Ould Tah, alisema taasisi hiyo itaendelea kusaidia nchi za Afrika kubadilisha fursa za miundombinu kuwa miradi inayoweza kufadhiliwa na kutekelezwa kwa ufanisi.

Amesema katika muongo wa pili wa Africa50, kipaumbele kitakuwa kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi, kuhamasisha mitaji na kuimarisha ushirikiano kati ya serikali, taasisi za fedha na sekta binafsi.

Mkutano huo pia ulihusisha mjadala wa mawaziri kutoka Tanzania, Msumbiji, Nigeria na Senegal kuhusu matumizi ya gesi asilia, maendeleo ya viwanda, kuongeza thamani ya rasilimali na ujenzi wa miundombinu ya kikanda.

Katika mjadala huo ilielezwa kuwa zaidi ya Waafrika milioni 600 bado hawana huduma ya umeme, huku Tanzania ikitajwa kuongeza upatikanaji wa nishati safi ya kupikia kutoka asilimia sita mwaka 2021 hadi asilimia 28 mwaka 2026.

Sambamba na mkutano huo, Tanzania ilisaini makubaliano mbalimbali ya ushirikiano yanayolenga kupanua huduma za matibabu ya figo, kuendeleza miradi ya usafirishaji wa umeme kwa ubia wa sekta ya umma na binafsi, pamoja na kuongeza matumizi ya gesi asilia katika shughuli za viwanda.

Makubaliano hayo yanahusisha Africa50, Wizara ya Afya, Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) pamoja na kampuni ya TAQA Arabia.

Akihitimisha hotuba yake, Rais Samia aliipongeza Africa50 kwa mchango wake katika kuendeleza ajenda ya miundombinu barani Afrika na kusisitiza kuwa makubaliano yote yaliyofikiwa yanapaswa kutekelezwa kwa haraka ili yaweze kuleta manufaa ya moja kwa moja kwa wananchi.



 




Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu (MB) (Mwenye Suti) akisikiliza maelezo ya Huduma zinazopatikana katika banda la Mfuko wa PSSSF katika Maonesho ya Kilimo (Nanenane) Kanda ya Kusini yanayoendelea katika Viwanja vya Ngongo Manispaa ya Lindi Agosti 5, 2026

Mkurugenzi wa Utawala na Uendeshaji wa GST,  Neema  Mhagama akizungumza na waandishi wa habari  alipotembelea banda la GST katika Maonesho ya  Kilimo ya Kimatiafa Nane Nane yanayoendelea  kwenye Viwanja vya Dkt.John Samwel Malecela ,Nzuguni jijini Dodoma,
Na Mwandishi Wetu

TAASISI ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) imesema inaendelea kuwekeza katika mafunzo na ushirikiano na taasisi mbalimbali za kitaifa na kimataifa, ikiwa ni sehemu ya mikakati ya kuimarisha uwezo wa kitaalamu katika tafiti za jiosayansi na uchunguzi wa sampuli maabara.

Akizungumza wakati wa ziara katika Banda la GST kwenye Maonesho ya Kilimo ya Kimataifa Nane Nane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samwel Malecela, Nzuguni jijini Dodoma, Mkurugenzi wa Utawala na Uendeshaji wa GST, Neema Mhagama, amesema taasisi hiyo imekuwa ikiwajengea uwezo watumishi wake kupitia mafunzo na ushirikiano wa kitaalamu na taasisi za ndani na nje ya nchi

Amesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha GST inaendelea kuendana na mabadiliko ya teknolojia na kutumia mbinu za kisasa katika kufanya tafiti za jiosayansi pamoja na uchunguzi wa sampuli mbalimbali za miamba na madini.


“Ushirikiano huu umeendelea kuimarisha uwezo wa wataalamu wetu kwa kubadilishana uzoefu na teknolojia, jambo ambalo linaongeza tija katika shughuli za taasisi na kuchangia maendeleo ya Sekta ya Madini nchini,” amesema Mhagama.
Kwa mujibu wa Mhagama, GST imekuwa ikishirikiana na taasisi mbalimbali za ndani, zikiwemo Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), pamoja na taasisi za kimataifa kutoka Uingereza, Finland, Korea Kusini na pamoja na China.


Amesema kupitia mafunzo, programu za kubadilishana uzoefu na ushirikiano wa kitaalamu, wataalamu wa GST wameweza kupata maarifa na teknolojia mpya zinazochochea ubunifu na kuongeza ufanisi katika tafiti za jiosayansi

Ameongeza kuwa maarifa hayo yamekuwa na mchango katika kuboresha huduma zinazotolewa kwa wachimbaji, wawekezaji na wadau wengine wa Sekta ya Madini.

Aidha, Mhagama amewahimiza wadau wa Sekta ya Madini kutumia wataalamu wa GST katika shughuli zao za uchimbaji ili kupata taarifa sahihi kuhusu miamba, namna bora ya uchimbaji pamoja na uchukuaji na uchunguzi wa sampuli za miamba.

“Tunawahimiza wadau kutumia wataalamu wa GST ili kupata taarifa sahihi zitakazowawezesha kufanya uchimbaji wenye tija na kupunguza changamoto zinazoweza kujitokeza katika shughuli za uchimbaji,” amesema.

Vilevile, Mhagama amewaalika wananchi na wadau mbalimbali waliopo Dodoma na maeneo mengine nchini kutembelea Banda la GST katika Maonesho ya Nane Nane yanayoendelea jijini Dodoma, ili kupata elimu na kujifunza masuala mbalimbali yanayohusu jiolojia na madini.

Na Mwandishi Wetu
NIC Insurance imewahimiza wananchi kutumia fursa ya Bima ya Maisha ya Majaliwa katika kujiwekea malengo ya kifedha yatakayowasaidia baada ya kufikia muda walioujiwekea.

Hayo yamesemwa na Afisa Bima wa NIC Insurance, Thecla Mtege, wakati akizungumza na wananchi waliotembelea Banda la NIC Insurance katika Maonesho ya Kilimo ya Kimataifa yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samwel Malecela, Nzuguni jijini Dodoma.

Thecla amesema kupitia Bima hiyo, mwananchi anaweza kujiwekea malengo ya kifedha kwa muda anaouona unafaa, ikiwamo miaka mitano, 10 au zaidi, huku akichangia kiasi cha fedha anachokimudu kila mwezi.

Amesema utaratibu huo unamwezesha mwananchi kuweka akiba kwa ajili ya kutimiza malengo yake ya baadaye, kulingana na kiwango na muda alioujiwekea.

“Bima ya Maisha ya Majaliwa inamwezesha mwananchi kuchangia kiasi kidogo cha fedha kila mwezi kulingana na uwezo wake na malengo aliyojiwekea,” amesema Thecla.

Aidha, amesema iwapo mwananchi aliyekata Bima hiyo atafariki kabla ya kukamilisha muda wa Bima, NIC Insurance italipa kiasi cha Bima kwa wategemezi waliotajwa kwenye taarifa za Bima kwa kiwango kilekile kilichoainishwa.

Amesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha familia ya mwananchi aliyejiwekea mpango huo inaendelea kupata ulinzi wa kifedha hata endapo atafariki kabla ya kufikia muda wa kukamilisha malengo yake.

Dar es Salaam, Agosti 5, 2026 – Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira Tanzania (TRAMEPRO) limetoa wito kwa Serikali, wataalamu wa afya, wataalamu wa tiba asili, wakunga, wadau wa mazingira na jamii kwa ujumla kushirikiana katika kulinda afya na uhai wa mama na mtoto, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Wiki ya Unyonyeshaji Duniani yanayoendelea kuanzia Agosti 1 hadi 7, 2026.


Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, TRAMEPRO limesema linaungana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Shirika la Afya Duniani (WHO), UNICEF, Wizara ya Afya na wadau wengine wa afya duniani katika kuhamasisha unyonyeshaji wa maziwa ya mama kama njia muhimu ya kuboresha afya ya watoto na akina mama.

Shirika hilo limeeleza kuwa Wiki ya Unyonyeshaji Duniani ilianzishwa mwaka 1992 na World Alliance for Breastfeeding Action (WABA) kwa ushirikiano na WHO na UNICEF, kufuatia Azimio la Innocenti la mwaka 1990, lenye lengo la kulinda, kuhamasisha na kuunga mkono unyonyeshaji wa maziwa ya mama duniani.

Kwa mujibu wa TRAMEPRO, unyonyeshaji wa maziwa ya mama ni moja ya njia bora za kupunguza vifo vya watoto wachanga na kuboresha afya ya mama. Shirika hilo limeunga mkono mapendekezo ya WHO yanayosisitiza mtoto kuanza kunyonya ndani ya saa moja baada ya kuzaliwa, kupewa maziwa ya mama pekee kwa miezi sita ya kwanza, na kuendelea kunyonyeshwa pamoja na vyakula vya nyongeza hadi miaka miwili au zaidi.

TRAMEPRO pia limebainisha kuwa Tanzania hupata wastani wa watoto kati ya milioni 2.2 na 2.4 wanaozaliwa hai kila mwaka, huku Afrika ikichangia takribani asilimia 70 ya vifo vya akina mama duniani. Aidha, zaidi ya watoto wachanga milioni moja hufariki kila mwaka barani humo kutokana na sababu zinazoweza kuzuilika, ikiwemo kuzaliwa kabla ya wakati, maambukizi, kukosa hewa wakati wa kuzaliwa na utapiamlo.

Shirika hilo limeeleza kuwa afya ya mama na mtoto haiwezi kutenganishwa na mazingira bora, likisisitiza umuhimu wa upatikanaji wa maji safi, lishe bora, usafi wa mazingira, hewa safi na uhifadhi wa bioanuwai. Pia limefafanua kuwa mimea tiba, ambayo ni sehemu ya tiba asili, hutegemea mazingira salama na uhifadhi wa misitu pamoja na vyanzo vya maji.

Katika taarifa hiyo, TRAMEPRO limetoa wito maalumu kwa wataalamu wa tiba asili, wakunga wa jadi na wakunga wataalamu kuzingatia sheria, maadili ya taaluma na ushahidi wa kisayansi katika utoaji wa huduma. Pia limewahimiza kuwashauri wajawazito kuhudhuria kliniki mapema, kujifungulia katika vituo vya afya, kutambua dalili za hatari mapema na kushirikiana kwa karibu na wataalamu wa afya ili kuokoa maisha ya mama na mtoto.

Aidha, shirika hilo limetoa wito kwa Serikali kuendelea kuwekeza katika huduma za afya ya uzazi, kuongeza idadi ya wakunga na wahudumu wa afya, kuimarisha lishe, chanjo, maji safi na usafi wa mazingira, pamoja na kuwekeza katika tafiti za tiba asili salama.

TRAMEPRO pia limealika Wizara, taasisi za Serikali, mashirika ya kimataifa, asasi za kiraia, vyuo vikuu, taasisi za utafiti, sekta binafsi na washirika wa maendeleo kushirikiana katika kuendeleza tafiti, elimu ya afya, uhifadhi wa mimea tiba na ulinzi wa mazingira kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Shirika hilo limemalizia kwa kusisitiza kuwa kulinda afya ya mama na mtoto ni jukumu la kila mwananchi na kwamba ushirikiano kati ya sekta ya afya, tiba asili na uhifadhi wa mazingira ni msingi wa kujenga Taifa lenye watoto wenye afya, akina mama salama na maendeleo endelevu.


Na Avila Kakingo
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan, amesema Afrika inapaswa kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya miundombinu na uwekezaji ili kufikia malengo ya maendeleo na kuhakikisha wananchi wananufaika moja kwa moja na matokeo yake.

Akizungumza jijini Dar es Salaam katika ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Wanahisa wa Africa50 na Jukwaa la Miundombinu Afrika, Dk. Samia amesema bara hilo limekuwa na maono na mipango mbalimbali ya maendeleo kwa muda mrefu, lakini sasa kinachohitajika ni utekelezaji wa miradi yenye matokeo yanayoonekana katika maisha ya wananchi.

Amesema wananchi hawapimi maendeleo kwa ahadi au matamko, bali kwa uwepo wa miundombinu bora kama barabara, reli, bandari, nishati ya uhakika na mifumo ya kidijitali inayochochea biashara, kuvutia uwekezaji na kuboresha huduma za kijamii.

"Ni wakati wa kugeuza mawazo kuwa miradi, ushirikiano kuwa uwekezaji na fursa za Afrika kuwa ustawi wa watu wetu," amesema.

Amesema dunia inaendelea kukabiliwa na changamoto mbalimbali zikiwemo mabadiliko ya tabianchi, misukosuko ya uchumi wa dunia na upungufu wa mitaji, hali inayolazimu Afrika kujitegemea zaidi kwa kuwekeza katika rasilimali zake na kuongeza biashara ndani ya bara kupitia Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA).

Amesema Tanzania imeendelea kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika miundombinu ikiwemo upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam, ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR), viwanja vya ndege pamoja na miradi ya barabara na nishati ili kuimarisha nafasi yake kama lango la biashara kwa nchi zisizo na bandari kama Burundi, Rwanda, Uganda, Zambia na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).

Kuhusu sekta ya nishati, amesema Tanzania imeongeza uzalishaji wa umeme kupitia maji, gesi asilia na vyanzo vingine vya nishati safi ili kuhakikisha upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa viwanda na shughuli nyingine za kiuchumi.

"Serikali inaendelea kuimarisha miundombinu ya kidijitali ili kuongeza ubunifu, huduma za kifedha na fursa kwa vijana na wajasiriamali," amesema.

Akizungumzia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, amesema Serikali inalenga kujenga uchumi wa kisasa unaoshindana kimataifa, huku sekta binafsi ikitarajiwa kutekeleza zaidi ya asilimia 70 ya uwekezaji unaohitajika katika kipindi cha miaka 25 ijayo.

Amewahimiza wawekezaji na taasisi za kifedha kushirikiana na Tanzania katika sekta mbalimbali zikiwemo usafirishaji, nishati, viwanda, usafirishaji wa mizigo na uchakataji wa bidhaa ili kuongeza thamani ya rasilimali za Afrika.

Aidha, ameipongeza Africa50 kwa mchango wake katika kufadhili na kuharakisha utekelezaji wa miradi ya miundombinu barani Afrika, akisema taasisi hiyo ni mfano wa namna Waafrika wanavyoweza kushirikiana kujenga mustakabali wa bara lao.

Katika mkutano huo, hati mbalimbali za makubaliano zilisainiwa zikiwemo za ushirikiano katika huduma za matibabu ya figo, miradi ya usambazaji wa umeme pamoja na mpango wa usafirishaji wa gesi asilia kwenda katika nchi nyingine za Afrika.

Kwa upande wake, Naibu wa Rais wa Kenya, Prof. Kithure Kindiki, amesema maendeleo ya viwanda na uchumi yanategemea upatikanaji wa nishati ya uhakika, nafuu na inayowafikia wananchi kwa urahisi, huku akisisitiza umuhimu wa kuwa na miundombinu mikubwa ya uzalishaji na usambazaji wa nishati pamoja na sera zinazovutia uwekezaji.

Naye Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar, amesema kaulimbiu ya mkutano huo ya "Kutoka Maono hadi Matokeo" inalenga kuhimiza ushirikiano kati ya Serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo ili kuhakikisha miradi mikubwa inatekelezwa kwa ufanisi na kuleta matokeo yanayoonekana.

Kwa upande wake, Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika na Mwenyekiti wa Bodi ya Africa50, Dk. Sidi Ould Tah, amesema maadhimisho ya miaka 10 ya taasisi hiyo yanaashiria mafanikio makubwa katika kuhamasisha uwekezaji wa miundombinu barani Afrika, huku akisisitiza kuwa hatua inayofuata ni kuharakisha utekelezaji wa miradi badala ya kubaki kwenye maono pekee.






Matukio mbalimbali katika picha 

Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) imesema ushiriki wake katika Maonesho ya Nanenane 2026 unalenga kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi sahihi ya dawa za mifugo, taratibu za udhibiti wa bidhaa za dawa na vifaa tiba, pamoja na kuhamasisha uwekezaji katika viwanda vya kutengeneza dawa za mifugo nchini.

Akizungumza katika mahojiano maalum yaliyofanyika kwenye banda la TMDA katika Maonesho ya Nanenane yanayoendelea kitaifa jijini Dodoma, Meneja wa TMDA Kanda ya Kati, Sonia Mkumbwa, amesema mamlaka hiyo imeona ni muhimu kushiriki maonesho hayo ili kuwafikia wadau wa sekta ya kilimo na mifugo pamoja na wananchi kwa ujumla.

Amesema TMDA ina jukumu la kudhibiti ubora, usalama na ufanisi wa dawa na vifaa tiba vinavyotumika kwa binadamu na mifugo, hivyo maonesho hayo ni fursa muhimu ya kutoa elimu kuhusu huduma na majukumu ya mamlaka hiyo.

“Moja ya majukumu yetu makubwa ni kutoa elimu kwa umma. Tunatumia maonesho haya kuwaeleza wananchi matumizi sahihi ya dawa za mifugo, pamoja na kushirikiana na taasisi nyingine za umma, sekta binafsi na wajasiriamali katika kuimarisha huduma za afya ya mifugo,” amesema.

Mkumbwa ameeleza kuwa, TMDA ndiyo mamlaka yenye dhamana ya kusimamia uingizaji wa dawa za mifugo nchini, ambapo kila bidhaa inapaswa kusajiliwa na kupata kibali kabla ya kuingizwa nchini.

Amesema kabla ya usajili, mamlaka hufanya tathmini ya kina ili kuhakikisha bidhaa hizo zinakidhi viwango vya ubora, usalama na ufanisi, hatua inayolenga kulinda afya ya mifugo na watumiaji wa bidhaa zinazotokana na mifugo.

Aidha, amewataka wafugaji, wafanyabiashara na wadau wote wa sekta ya mifugo kuhakikisha wanatumia dawa zilizosajiliwa na kufuata taratibu zilizowekwa na TMDA.

Mbali na udhibiti wa dawa na vifaa tiba, Mkumbwa amesema TMDA inaendelea kuhamasisha wawekezaji kuanzisha viwanda vya kutengeneza dawa za mifugo na vifaa tiba nchini ili kuongeza uzalishaji wa ndani na kupunguza utegemezi wa bidhaa kutoka nje.

Amebainisha kuwa mamlaka hiyo ipo tayari kuwapa wawekezaji mwongozo na ushauri katika hatua zote za uanzishaji wa viwanda, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Serikali chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuimarisha uchumi wa viwanda na kuongeza thamani ya uzalishaji wa ndani.

Kwa upande wa huduma za uchunguzi wa maabara, Mkumbwa amesema TMDA ina maabara yenye ithibati ya Shirika la Afya Duniani (WHO), zinazofanya uchunguzi wa dawa za mifugo na vifaa tiba ili kuhakikisha bidhaa zinazotumika nchini zinakidhi viwango vinavyotakiwa.

Amesema huduma hizo zinapatikana katika makao makuu ya TMDA jijini Dodoma na katika maabara zake zilizopo Dar es Salaam.

Mkumbwa ametoa wito kwa wananchi, wafugaji na wawekezaji kutembelea banda la TMDA katika Maonesho ya Nanenane ili kupata elimu, ushauri na huduma mbalimbali zinazotolewa na mamlaka hiyo.

“Afya ya mifugo ni msingi wa usalama wa chakula na afya ya binadamu. Hivyo ni muhimu kuhakikisha bidhaa zote zinazotumika kutibu mifugo zinakuwa salama, bora na zenye ufanisi,” amesema.



 

Na OWM – TAMISEMI, Morogoro

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amewapongeza wakulima, wafugaji na wavuvi kwa mchango wao mkubwa uliowezesha Tanzania kufikia utoshelevu wa chakula wa zaidi ya asilimia 120, hatua inayodhihirisha mafanikio ya uwekezaji unaoendelea kufanywa na Serikali katika sekta za kilimo, mifugo na uvuvi.

Dkt. Mwigulu aliwasilisha pongezi hizo za Mhe. Rais Agosti 4, 2026, alipotembelea Maonesho ya Nane Nane Kanda ya Mashariki yanayofanyika katika Viwanja vya Nane Nane mkoani Morogoro.

 Katika ziara hiyo alijionea shughuli na ubunifu wa wakulima, wafugaji na wavuvi kutoka mikoa ya Morogoro, Dar es Salaam, Pwani na Tanga.

Amesema maonesho ya mwaka huu yanaongozwa na kaulimbiu isemayo, "Tambua Soko; Ongeza Tija Kutekeleza Dira 2050," ambayo inawahimiza Watanzania kuzalisha kwa kuzingatia mahitaji ya soko, kutumia teknolojia za kisasa, kuongeza ubora wa bidhaa na kuimarisha mnyororo wa thamani ili kufanya kilimo kuwa biashara yenye tija na mchango mkubwa katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

"Kwa nilichojionea kupitia maonesho ya mwaka huu, ninaziona dalili zote kwamba ifikapo mwaka 2050 malengo ya Dira ya Taifa tuliyojiwekea yatakuwa yamefikiwa, kwa kuwa tuko kwenye hatua nzuri ya utekelezaji katika sekta za kilimo, mifugo na uvuvi," amesema Dkt. Mwigulu.

Ameongeza kuwa ameridhishwa na ubora wa mazao mbalimbali yaliyooneshwa, ikiwemo nyanya, bilinganya na bidhaa nyingine zinazokidhi viwango vya masoko ya kimataifa, yakiwemo ya Marekani na Ulaya, jambo linaloashiria kuwa Tanzania ipo kwenye mwelekeo sahihi wa kuzalisha bidhaa zenye ushindani duniani.

Akizungumzia sekta ya mifugo na uvuvi, Dkt. Mwigulu amesema zimeendelea kuwa nguzo muhimu za uchumi wa taifa, akibainisha kuwa mchango wa sekta ya mifugo katika pato la taifa umeongezeka kutoka asilimia 2.3 hadi asilimia 6.2.

Ametoa mfano wa mafanikio ya wanaonufaika na sekta hiyo kwa kumtaja kijana mmoja mhitimu anayejihusisha na ufugaji wa kisasa, ambaye ameonesha ng'ombe mwenye uzito wa zaidi ya kilogramu 1,000 mwenye thamani ya takribani Shilingi Milioni 20. Aidha, amesema kijana huyo anafuga zaidi ya ng'ombe 200 na alipoulizwa na Waziri wa TAMISEMI kama anahitaji mkopo, alieleza kuwa hana uhitaji huo kutokana na mafanikio ya shughuli zake.

Awali, akitoa neno la utangulizi kabla ya Waziri Mkuu kuzungumza na wananchi pamoja na washiriki wa maonesho hayo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, alisema Waziri Mkuu alimpa jukumu la ulezi wa Mkoa wa Morogoro, hivyo alimkaribisha rasmi kama waziri mwenyeji wa mkoa huo, ambao ni mmoja wa mikoa inayounda Kanda ya Mashariki katika Maonesho ya Nane Nane.











Jumla ya taasisi za umma 54 zinatarajiwa kuwasilisha taarifa za utendaji wa uwekezaji mbele ya Kamati za Kudumu za Bunge kwa muda wa wiki tatu, katika mchakato unaolenga kuwezesha uchambuzi wa thamani na utendaji wa mitaji ya umma pamoja na utekelezaji wa mipango ya kimkakati ya taasisi husika.

Katika awamu hii iliyoanza Jumatatu, Agosti 3, 2026, taasisi hizo zimepangwa kuwasilisha taarifa zao mbele ya Kamati mbili za Kudumu za Bunge, ambapo 27 zitawasilisha mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) na nyingine 27 mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Umma (PAC).

Hadi Jumatano, Agosti 5, 2026, taasisi nne zilikuwa tayari zimewasilisha taarifa zao mbele ya Kamati. 

Taasisi hizo ni Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL), Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB), Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA) na Wakala wa Huduma za Ununuzi Serikalini (GPSA), huku Kamati zikionesha kuridhishwa na utendaji wa taasisi husika.

Uwasilishaji huo ni sehemu ya utekelezaji wa jukumu la kusimamia na kufuatilia utendaji wa uwekezaji wa Serikali kupitia taasisi na kampuni zilizo chini ya usimamizi wa Ofisi ya Msajili wa Hazina (OTR).

OTR inasimamia taasisi na kampuni 308, zikiwemo taasisi za umma 252 na kampuni 56 ambazo Serikali ina umiliki wa hisa chache, huku jumla ya uwekezaji katika taasisi na kampuni hizo ikiwa Sh92.3 trilioni.

Kaimu Msajili wa Hazina, Bi Lightness Mauki, alisema uwasilishaji huo unaipa Bunge fursa ya kupata picha ya kina kuhusu mwenendo wa uwekezaji wa mitaji ya umma.

“Uwasilishaji wa taarifa hizi ni moja ya utaratibu wa Bunge katika kusimamia Serikali, ikiwemo usimamizi wa uwekezaji wa mitaji ya umma,” alisema Bi. Mauki, ambaye pia ni Mkurugenzi wa Usimamizi wa Utendaji wa Mashirika ya Kibiashara.

Taarifa hizo huwezesha kuangalia thamani ya mitaji, mapato na matumizi, faida, hali ya mizania pamoja na utekelezaji wa mipango ya kimkakati ya taasisi husika, ikiwa ni msingi wa uwajibikaji na utawala bora,” alisema Mauki.

Uwasilishaji wa taarifa hizo unafanyika kwa mujibu wa Kanuni ya 11 ya Kanuni za Kudumu za Bunge, inayozipa Kamati jukumu la kuchambua na kubaini iwapo utekelezaji wa miradi ya uwekezaji wa umma unafanyika kwa ufanisi na kwa kuzingatia taratibu, sheria na miongozo ya biashara.

Kwa mujibu wa Bi. Mauki, Kamati pia inachambua na kujadili taarifa zinazohusu uwekezaji katika mashirika ya umma na kampuni ambazo Serikali inamiliki hisa.

Alisema OTR inaratibu mchakato huo na kuhakikisha taarifa zinazowasilishwa zinaakisi kwa usahihi na uwazi hali halisi ya utendaji wa taasisi na mashirika ya umma, ili kuwezesha Kamati za Bunge kufanya uchambuzi na kutoa ushauri na maelekezo yanayolenga kuimarisha utendaji.

“Jukumu la Ofisi ya Msajili wa Hazina katika zoezi hili ni kuratibu na kuhakikisha taarifa za mashirika ya umma zinakuwa na ukweli na uwazi wa hali halisi wa utendaji wa taasisi hizo ili kutoa fursa kwa Kamati za Bunge kushauri na kuelekeza katika masuala mbalimbali yanayolenga kuimarisha utendaji wa mashirika ya umma,” alifafanua Mauki.

Uwasilishaji wa taarifa za mashirika hayo ulitanguliwa na uwasilishaji wa Taarifa kuhusu hali ya Uwekezaji wa Umma hadi kufikia Mwaka 2024/2025 mbele ya PIC.

Taarifa hiyo, iliyowasilishwa na Bi. Mauki, ilijikita katika kuonesha hali ya uwekezaji wa Serikali ndani na nje ya nchi, mgawanyo wa uwekezaji katika mashirika ya umma, mapato yasiyo ya kodi ya mashirika na taasisi za umma, mikopo ya mashirika na taasisi za umma pamoja na taarifa za dhamana na misaada katika mashirika hayo.

Mchakato huo unaendelea kutoa fursa kwa Bunge kuchambua mwenendo wa uwekezaji wa mitaji ya umma na kutoa maoni na maelekezo yanayoweza kusaidia kuimarisha utendaji, uwajibikaji na matumizi yenye tija ya rasilimali za umma. 




Mamlaka ya Hifadhi ya eneo la Ngorongoro (NCAA) kwa kushirikiana na Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imetoa elimu kwa jamii ya Ngorongoro kuhusu mfuko wa Ngorongoro Scholarship Fund unaolenga kuwezesha wanafunzi wanaoishi ndani ya hifadhi ya Ngorongoro kupata fursa ya masomo ya elimu ya juu kupitia ufadhili Ngorongoro Fund.

Elimu hiyo iliyotolewa katika ofisi za Ngorongoro ilijumuisha wadau muhimu wanaoguswa na mpango huo ambao ni viongozi wa jamii, wanafunzi pamoja na wadau mbalimbali ambao wamepewa uelewa kuhusu vigezo vya mkopo, sifa za waombaji pamoja na kupitia na kujadili mwongozo wa programu ya Ngorongoro Scholarship Fund.

Katika kikao hicho, viongozi wa jamii wamepongeza hatua ya Mamlaka ya kushirikiana na HESLB katika kuandaa na kuboresha mwongozo wa mfuko huo, wakieleza kuwa utasaidia kuweka utaratibu unaozingatia usawa, uwazi na mahitaji ya wakati katika kuwawezesha wanafunzi wenyeji kupata fursa za elimu ya juu.

Mwenyekiti wa Baraza la Wafugaji Ngorongoro, Mhe. Edward Maura, aliipongeza Mamlaka ya Ngorongoro na HESLB kwa kutoa elimu kuhusu Ngorongoro Scholarship Fund hasa jinsi wanufaika wanavyoweza kutambua fursa, kujaza fomu na kufuata taratibu za kuomba ufadhili.

“Tunawapongeza Ngorongoro na Bodi ya Mikopo kwa kutoa elimu hii kwa jamii na wanafunzi na kusaidia kuwaondolea wanafunzi changamoto na uelewa mdogo wa namna ya kuomba na kupata mikopo huu, tunaamini maamuzi haya ya Serikali yanalenga kuimarisha mahusiano kati ya jamii na Ngorongoro na tunaamini wanafunzi na jamii watatumia fursa zinazotolewa kwa kuzingatia taratibu zilizowekwa” alisema Mh. Maura.

Utekelezaji wa program hii unalenga kuimarisha ushirikiano na kuboresha huduma za jamii kwa wananchi wa Ngorongoro ambapo elimu wanayopata itasaidia ushiriki wao katika program za uhifadhi endelevu na kuvutia wageni kupitia vivutio vya utalii vilivyopo.











Top News