Na Mwandishi Wetu

Waandishi wa Habari watakaoshiriki Tuzo za Uandishi wa Habari na Makala za Maendeleo (Samia Kalamu Awards - SKA) 2026 wamelazimika kukidhi sharti la kuwa na ithibati kutoka Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), hatua inayolenga kuimarisha weledi, uwajibikaji na ushindani wa haki katika taaluma hiyo.

Akizindua rasmi mchakato wa kupokea kazi za kushindanishwa, Jumapili tarehe 31 Mei, 2026, jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa SKA, Mha. Peter Mwasalyanda, amesema maandalizi ya mwaka huu yanazingatia maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuendelea kutambua mchango wa Waandishi wa Habari za maendeleo nchini.
Mwasalyanda amesema ili kuhakikisha uadilifu, uwazi na ushindani wa haki, maandalizi ya tuzo hizo yanahusisha pia Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) kama mdau muhimu katika kusimamia weledi na maadili ya taaluma ya uandishi wa habari.

“Tuzo hizi zinalenga kutambua, kuthamini na kuhamasisha uzalishaji wa maudhui ya ndani yenye ubora, yanayochangia kuelimisha, kuhabarisha na kuburudisha, na kuimarisha taswira chanya ya Taifa kupitia habari za maendeleo,” amesema.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, amesema tofauti na msimu wa kwanza wa tuzo hizo, mwaka huu washiriki wanapaswa kuhakikisha wamekidhi sharti la ithibati.

“Mtakumbuka Msimu wa kwanza wa Samia Kalamu mambo ya JAB hayakuwepo, kwa hiyo waandishi walishiriki wote bila kujali vigezo vya Ithibati lakini mwaka huu kuna hiki kigezo cha kuwa na ithibati kwa hiyo niwashauri basi wote wanaoshiriki kwenye hizi tuzo wahakikishe wanakuwa na ithibati, wamethibitishwa na Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari.” Amesema Wakili Kipangula na kuongeza;
“Ni muhimu sana kwa sababu ni takwa la kisheria na kitu ambacho hatuwezi kukikwepa. Nawahamasisha tushiriki wote kwa sababu isionekane ni tuzo za watu fulani tu, kila mmoja awasilishe kazi zake,” amesema Kipangula.

Kwa mujibu wa vigezo vya ushiriki vilivyotangazwa, Waandishi wa Habari wa Tanzania Bara wanatakiwa kuwa wamethibitishwa na JAB, huku kwa Zanzibar washiriki wakitakiwa kuwa na kitambulisho cha Mwandishi wa Habari (Press Card).

Tuzo hizo zimeanza kupokea kazi kuanzia Mei 31 hadi Juni 30, 2026 na zinatarajiwa kutolewa kati ya Oktoba na Desemba mwaka huu.

 


Na Mwandishi wetu, Iringa.

Wapiga Kura 222,218 walioandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura watashiriki kwenye uchaguzi mdogo wa Ubunge katika Jimbo la Isimani lililopo Halamashauri ya Wilaya ya Iringa Mkoani Iringa na Kata 12 za Tanzania Bara.
 
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele ameyasema hayo leo Mei 31, 2026 Mkoani Iringa wakati akisoma risala maalum kuhusu uchaguzi katika jimbo na kata husika utakao fanyika kesho Juni 01, 2026 na kusema kuwa jumla ya vituo 628 vya Kupigia Kura vitatumika.
 
“wapiga kura 89,753 wapo kwenye Jimbo la Ismani na wapiga kura 132,465 wapo kwenye kata 12 zitakazofanya uchaguzi mdogo na vituo 277 vipo kwenye Jimbo la Ismani na vituo 351 vipo kwenye kata 12 zitakazofanya uchaguzi mdogo.,”amesema Jaji Mwambegele.
 
Aidha, amesema Katika Uchaguzi huu, jumla ya wagombea 108 kutoka katika vyama vya siasa 17 wanawania nafasi wazi ya ubunge na udiwani katika maeneo niliyoyataja.

“Jimbo la Ismani lina wagombea 17 wa nafasi ya Ubunge ambapo kati ya wagombea hao wagombea nane (08) sawa na asilimia 47.06 ni wanaume na wagombea tisa (09) sawa na asilimia 52.94 ni wanawake. Kata 12 zinazofanya uchaguzi mdogo wa udiwani zina jumla ya wagombea 91 ambapo kati ya hao wagombea 61 sawa na asilimia 67.03 ni wanaume na wagombea 30 sawa na asilimia 32.97 ni wanawake.” alisema Jaji Mwambegele.

“Natumia fursa hii kuvikumbusha Vyama vya Siasa vinavyoshiriki uchaguzi kesho Juni 01, 2026 kuzingatia wajibu wao wa kuweka mawakala katika vituo vyote vya zoezi la kupiga, kuhesabu na kujumlishia kura. Wasimamizi wa uchaguzi katika Jimbo na Kata husika, wamekamilisha taratibu zinazoweka mazingira yanayowawezesha mawakala wa vyama vya siasa kufuatilia mchakato mzima wa uchaguzi,”alisema Jaji Mwambegele.
 
Amesema, mawakala hao, wanawajibika katika kulinda maslahi ya vyama na wagombea wao. Hivyo, wanapaswa kuzingatia Sheria, Kanuni, taratibu za Uchaguzi na maelekezo ya Tume katika utekelezaji wa majukumu yao vituoni.
 
Jaji Mwambegele amesema vituo vitafunguliwa saa 01:00 asubuhi na kufungwa saa 10:00 jioni na kwamba ifikapo muda wa kufunga kituo saa 10:00 kamili jioni, kama wapiga kura bado wapo kwenye mistari, mlinzi wa kituo atasimama nyuma ya mtu wa mwisho na zoezi la upigaji kura litaendelea hadi wapiga kura walio kwenye mstari watakapomalizika.
 
“Baada ya kumaliza kupiga kura, mpiga kura anatakiwa kuondoka eneo la kituo cha kupigia kura; na Mpiga kura awapo kituoni, anatakiwa kufuata maelekezo yote atakayopewa na karani mwongozaji wapiga kura,”amesema Jaji Mwambegele.
 
Kwa mpiga kura ambaye ameandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na taarifa zake zipo katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura lililopo katika kituo husika, lakini amepoteza kadi yake au kadi yake imeharibika, ataruhusiwa kupiga Kura kwa kutumia moja wapo ya vitambulisho cha Taifa NIDA, Leseni ya udereva au Pasi ya kusafiria (Passport).

Kata 12 zitakazo fanya uchaguzi ni Mzimuni iliyopo Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni; Zongomera, Halmashauri ya Manispaa ya Kahama; Itilo, Halmashauri ya Mji Nzega; Ketare, Halmashauri ya Mji Tarime na Nyumbigwa, Halmashauri ya Mji Kasulu. 

Nyingine ni Kata ya Kala iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi; Ziba, Halmashauri ya Wilaya Igunga; Kamsisi, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele; Nyamugali, Halmashauri ya Wilaya ya Buhigwe; Namasakata Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru; Bwongera, Halmashauri ya Wilaya ya Chato na Kibiti, Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti.
Cambridge, Uingereza Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya NMB, Ruth Zaipuna, amesema hatua inayofuata ya ukuaji wa Afrika itategemea taasisi zinazoaminika, mitaji ya muda mrefu na mifumo jumuishi, baada ya kuwasilisha hadithi ya mageuzi ya sekta ya benki Tanzania katika Cambridge Africa Business Conference 2026.

Akizungumza katika kongamano hilo lililoandaliwa na Cambridge Judge Business School, University of Cambridge, chini ya kaulimbiu ya “Kujenga Mustakabali wa Afrika: Mitaji, Ubunifu na Ukuaji wa Pamoja wa Bara la Afrika,” Zaipuna aliitumia safari ya NMB kama mfano wa taasisi ya Afrika inayoweza kuvutia mtaji, kuchochea ubunifu na kujenga uaminifu.

“Mustakabali wa Afrika hautaletwa kwetu na wengine; utajengwa na sisi wenyewe kupitia mifumo jumuishi, taasisi zinazoaminika na nidhamu ya kuleta matokeo chanya na endelevu kwa vizazi vijavyo,” alisema.

Zaipuna alieleza mageuzi ya NMB kutoka matawi 97, wateja takribani 600,000 na amana za Sh bilioni 150 mwaka 1997 hadi zaidi ya wateja milioni 10 leo. Alisema kati ya mwaka 2021 na 2025, NMB imewekeza zaidi ya Sh bilioni 230 katika miundombinu ya kidijitali, usalama wa mifumo, teknolojia za kiotomatiki na uwezo wa matumizi ya takwimu, huku zaidi ya asilimia 98 ya miamala yote sasa ikifanyika nje ya matawi kupitia njia za kidijitali na mbadala.

Katika mjadala huo, Mtaalamu wa Fedha (Structured Finance) kutoka AfDB, Eghosa Giwa Osaige, alisema kuimarisha uaminifu na kupunguza gharama za vihatarishi ni muhimu katika kuongeza mtiririko wa mitaji kuelekea Afrika.

Mkurugenzi wa Uwekezaji wa BII, Jumai Hadiza Mohammed, alisema hati fungani za kijamii na uendelevu za NMB zinatoa mfano imara kwa benki za Afrika kuhusu namna ubunifu, ubia na masoko ya mitaji vinavyoweza kufungua uwekezaji kwa kiwango kikubwa.


Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu wa NMB Bank Plc, Ruth Zaipuna, akitoa hotuba kuu katika Cambridge Africa Business Conference 2026 katika Chuo Kikuu cha Cambridge, ambako aliwasilisha safari ya mageuzi ya NMB na mchango wake katika uchumi wa Tanzania.






 

Na Janeth Raphael -MichuziTv Singida 

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, ameagiza kuchukuliwa hatua kali za kisheria dhidi ya watumishi wote wa umma watakaobainika kuhusika na ubadhirifu wa fedha za Serikali, akisisitiza kuwa tabia ya kuwahamisha badala ya kuwakamata imekuwa ikichangia kuendelea kwa vitendo vya wizi katika maeneo mbalimbali nchini.

Dkt. Mwigulu ametoa kauli hiyo leo Mei 31, 2026 wakati akizungumza na wananchi wa Itigi mkoani Singida, ambapo ameeleza kuwa Serikali haitavumilia watumishi wanaotumia nafasi zao vibaya kwa kuiba mali na fedha za umma zilizotokana na kodi za wananchi.

Amesema watumishi wanaobainika kufanya ubadhirifu hawapaswi kuhamishwa kutoka kituo kimoja cha kazi kwenda kingine kwani hatua hiyo haina tija, badala yake huwapa nafasi ya kuendelea kufanya vitendo hivyo katika maeneo mapya wanayopelekwa.

“Mwizi wala msimuhamishe. Mkishamhamisha anaenda kuiba na huko. Wale ambao walishahamishwa, kule walikopelekwa RPC wa huko awakamate,” alisema Waziri Mkuu huku akipigiwa makofi na wananchi waliohudhuria mkutano huo.

Katika hotuba yake, Dkt. Mwigulu alionesha kusikitishwa na baadhi ya watumishi wa umma wanaoshindwa kutambua dhamana waliyopewa na wananchi, akibainisha kuwa wengi wao wamepata elimu kwa gharama za Serikali kupitia kodi za Watanzania na baadaye kupewa nafasi za kazi ili kulitumikia taifa.

Amesema ni jambo la kushangaza kuona baadhi yao wakitumia nafasi hizo kwa manufaa binafsi badala ya kuwahudumia wananchi kwa uadilifu na uzalendo.

“Kuna watu hawamwogopi hata Mungu. Umesoma kwa kodi za Watanzania, umepata nafasi ya kuwatumikia wenzako, lakini unaamua kuwaibia. Wakati huo huo kuna vijana wengi wenye sifa wanaosubiri nafasi za ajira,” alisema.

Waziri Mkuu ameongeza kuwa Serikali inaendelea kupambana na vitendo vya rushwa, ubadhirifu na matumizi mabaya ya fedha za umma ili kuhakikisha rasilimali za nchi zinatumika kwa manufaa ya wananchi wote.

Aidha, alihoji mantiki ya kuendelea kuwahamisha watumishi wanaotuhumiwa kwa ubadhirifu huku Serikali ikibeba gharama za uhamisho wao, ikiwemo posho na nauli, jambo alilosema halina tija katika mapambano dhidi ya wizi wa mali za umma.

“Baada ya kuiba unataka tukuhamishe na tukulipie nauli ya kuhama. Hata hizo sheria tutazirejea. Mimi sichukii watu, lakini nachukia wizi,” alisisitiza.

Kauli ya Waziri Mkuu imekuja wakati Serikali ikiendelea kusisitiza uwajibikaji, uwazi na nidhamu katika utumishi wa umma, huku ikitaka fedha za wananchi zilindwe na kutumika ipasavyo kwa ajili ya kuharakisha maendeleo na kuboresha huduma za kijamii nchini.

Wakazi wa Itigi waliohudhuria mkutano huo walimpongeza Waziri Mkuu kwa msimamo wake dhidi ya ubadhirifu, wakieleza kuwa hatua kali dhidi ya wahusika zitasaidia kuongeza uwajibikaji na kuimarisha imani ya wananchi kwa taasisi za umma


Na Janeth Raphael MichuziTv Itigi - Singida

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, ameielekeza Sekta ya Ardhi kujitathmini kwa kina na kuchukua hatua za haraka kurekebisha changamoto zinazoikabili, akieleza kuwa imeendelea kuwa chanzo kikubwa cha migogoro katika maeneo mbalimbali nchini.

Akizungumza na wananchi wa Itigi mkoani Singida leo Dkt. Mwigulu amesema kumekuwa na ongezeko la migogoro ya ardhi inayotokana na wizi, udanganyifu na uzembe wa baadhi ya watendaji, hali ambayo imekuwa ikisababisha wananchi kugombana na hata kuvuruga mshikamano wa kijamii.

Amesema migogoro hiyo imekuwa ikiwakosesha wananchi haki zao za msingi na kuathiri maendeleo ya jamii, huku baadhi ya wananchi wakijikuta wakipoteza ardhi zao kutokana na mifumo isiyo na ufanisi pamoja na vitendo vya rushwa vinavyohusishwa na baadhi ya watumishi wasio waadilifu.

Waziri Mkuu amesisitiza kuwa sekta hiyo inapaswa kufanya maboresho makubwa yatakayorejesha imani ya wananchi kwa kuhakikisha haki inatendeka kwa kila mwenye madai halali ya ardhi na kwamba serikali haitavumilia watendaji watakaobainika kushiriki vitendo vinavyozalisha migogoro hiyo.

Aidha, ameeleza kuwa ardhi ni rasilimali muhimu kwa maendeleo ya wananchi na taifa kwa ujumla, hivyo ni lazima isimamiwe kwa uadilifu, uwazi na weledi ili kuondoa malalamiko yanayoendelea kujitokeza katika maeneo mbalimbali nchini.

Dkt. Mwigulu ameonya kuwa migogoro ya ardhi ikiendelea kuachwa bila kutatuliwa inaweza kuathiri umoja wa wananchi na kuleta uhasama usio wa lazima, akisisitiza kuwa kila taasisi inayohusika na usimamizi wa ardhi inapaswa kutekeleza wajibu wake kwa kuzingatia sheria, kanuni na maslahi ya wananchi.

Aidha  amewataka viongozi na watendaji wa sekta hiyo kuhakikisha wanashughulikia kwa haraka kero za ardhi zinazowakabili wananchi ili kuimarisha amani, mshikamano na maendeleo ya taifa.



 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Mahmoud Thabit Kombo amekutana na  Jumuiya ya Diaspora ya Tanzania wanaoishi katika Jamhuri ya Korea na kuwahimiza kuendelea kuwa mabalozi wazuri wa Tanzania kwa kuitangaza nchi na fursa mbalimbali zilizopo katika sekta za uwekezaji, biashara na utalii. 

Akizungumza katika mkutano uliofanyika  jijini Seoul, Mei 31, 2026,  Balozi Dkt. Kombo alisisitiza umuhimu wa Watanzania wanaoishi nje kuifahamu vizuri nchi wanayoishi, ikiwemo tamaduni zake, lugha, sheria na mifumo ya kijamii ili waweze kujumuika kwa urahisi na kujenga uhusiano chanya unaoweza kuleta manufaa kwa Taifa. 

Alifafanua kuwa uelewa wa mazingira ya nchi mwenyeji huwasaidia diaspora kutambua fursa za kiuchumi na kijamii ambazo zinaweza kuwanufaisha wao pamoja na kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na nchi husika. 

Pia aliwahimiza kutumia majukwaa yao mbalimbali ya kitaaluma, kijamii na kibiashara kuitangaza Tanzania pamoja na fursa zinazopatikana katika nchi wanazoishi. Alibainisha kuwa kupitia mitandao na ushirikiano wao, diaspora wanayo nafasi kubwa ya kuvutia wawekezaji, watalii na washirika wa maendeleo kuwekeza na kushirikiana na Tanzania. 

Pia alitoa wito kwa Diaspora ambao ni wanafunzi wa elimu ya juu kujikita katika kufanya tafiti zinazolenga kutatua changamoto mbalimbali zilizopo nchini hususan katika sekta za afya, maji, elimu na mazingira. 

Kadhalika alitoa rai kwa Diaspora hao kuendelea kudumisha umoja, uzalendo na maadili mema ili kuendeleza taswira chanya ya Tanzania nchini Korea na kimataifa kwa ujumla. 

Kwa upande wake, Rais wa Jumuiya hiyo Bi. Eliusta Filikunjombe alieleza utayari wao wa kuendelea kushirikiana na Serikali katika kutangaza fursa na kuimarisha mahusiano ya watu kwa watu kati ya Tanzania na Jamhuri ya Korea. 

Awali akizungumza, Balozi wa Tanzania nchini Korea, Mhe. Noel Kaganda alisema idadi ya Diaspora wa Tanzania nchini humo inafikia 300 ambayo inajumuisha wafanyakazi, wafanyabiashara na wanafunzi. 

Mhe. Balozi Dkt Kombo yupo nchini Korea kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Korea na Afrika.














 

*Kinara wa Mageuzi Sekta ya Mafuta
*Ampongeza Rais Samia kwa Uchapakazi, Asema Tanzania Itashinda Changamoto ya Mafuta

Na Mwandishi Wetu
KATIKA ulimwengu wa biashara na uchumi wa kisasa, viongozi wachache huweza kuunganisha utaalamu, ubunifu, uzalendo na uwezo wa kuleta matokeo yanayoonekana ndani ya muda mfupi. Tanzania imebahatika kuwa na baadhi ya viongozi wa aina hiyo ambao kupitia maarifa yao wameendelea kutoa mchango mkubwa katika maendeleo ya taifa.

Miongoni mwao ni Dk. Sajad Habib Rai, mtaalamu mwenye uzoefu wa zaidi ya miaka 20 katika sekta ya mafuta, usafirishaji, manunuzi, teknolojia ya habari na usimamizi wa biashara.

Kupitia nafasi yake kama Meneja Mkazi wa Mansoor Industries Limited, Dk. Sajad ameonyesha uwezo mkubwa wa kusimamia operesheni za biashara huku akihakikisha kampuni inaendelea kukua na wakati huo huo kuunga mkono jitihada za Serikali za kuongeza mapato ya taifa.

Safari ya Mafanikio
Dk. Sajad, mwenye umri wa miaka 47, alianza safari yake ya kitaaluma kwa misingi ya nidhamu, kujifunza kwa bidii na kujituma kazini. Tangu akiwa kijana alionyesha uwezo mkubwa wa uongozi na hamu ya kutafuta suluhisho kwa changamoto mbalimbali zinazokabili taasisi na jamii.

Anasema Tanzania imebahatika kuwa na viongozi wenye maono tangu ilipopata uhuru mwaka 1961, na anaamini maendeleo ya taifa yanahitaji viongozi wanaoweka mbele maslahi ya wananchi na kufanya maamuzi yenye manufaa ya muda mrefu.

Rais Samia na Maendeleo ya Uchumi
Dk. Sajad anamtaja Rais Samia Suluhu Hassan kama mmoja wa viongozi waliobeba matumaini makubwa ya Watanzania katika kipindi hiki.

Kwa mujibu wake, uongozi wa Rais Samia umeleta ari mpya katika uwekezaji, utendaji wa serikali na usimamizi wa sekta mbalimbali za uchumi.

"Tunajivunia kuwa na kiongozi mwenye maono na anayefanya kazi kwa karibu na wananchi. Rais Samia ameonyesha uwezo mkubwa wa kuisimamia Tanzania katika kipindi kigumu cha changamoto za kiuchumi duniani," anasema.

Kauli hiyo inaakisi namna anavyounga mkono juhudi za serikali katika kuhakikisha uchumi wa taifa unaendelea kuwa imara licha ya changamoto zinazotokana na mabadiliko ya bei za mafuta na migogoro ya kimataifa.

Mbunifu wa Mfumo wa Kudhibiti Ukwepaji Kodi
Katika sekta ya mafuta, Dk. Sajad amejizolea sifa kama mmoja wa wataalamu wenye mawazo ya kimkakati yanayolenga kuleta uwazi na ufanisi katika biashara hiyo.

Kupitia uzoefu wake katika usafirishaji wa mafuta, usimamizi wa bohari na operesheni za biashara, aliweza kubaini mianya iliyokuwa ikisababisha Serikali kupoteza mapato kupitia ukwepaji wa kodi.

Moja ya michango yake mikubwa ni kupendekeza mfumo wa ulipaji kodi kwa waingizaji wa mafuta kabla bidhaa hizo hazijaingia sokoni. Mfumo huo ulisaidia kwa kiasi kikubwa kudhibiti mianya ya ukwepaji kodi na kuongeza uwezo wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kukusanya mapato kwa ufanisi zaidi.

Kwa mujibu wake, kabla ya kuanzishwa kwa mfumo huo kulikuwa na changamoto ya baadhi ya wafanyabiashara kutumia mianya ya kisheria kukwepa kodi. Hata hivyo, baada ya kuanzishwa kwa mfumo wa kukadiria kodi mapema kabla ya mafuta kuingia sokoni, hali ilibadilika kwa kiasi kikubwa.

"Mfumo huu umeongeza uwajibikaji na kusaidia kuondoa mazingira ya ujanja ujanja yaliyokuwa yanapelekea upotevu wa mapato ya taifa," anasema.

Anasisitiza kuwa mafanikio hayo yanaonyesha namna sekta binafsi inaweza kuwa mshirika muhimu wa serikali katika kuleta maendeleo ya taifa.

Kiongozi wa Biashara ya Mafuta
Katika Mansoor Industries Limited, Dk. Sajad anasimamia shughuli mbalimbali ikiwemo manunuzi, operesheni, usimamizi wa miradi na mipango ya biashara.

Kampuni hiyo inajishughulisha na biashara ya mafuta ya petroli na dizeli, huku pia ikimiliki Bohari ya Mafuta ya MOIL iliyopo Kigamboni, Dar es Salaam.

Uzoefu Mkubwa Katika TEHAMA
Mbali na sekta ya mafuta, Dk. Sajad ana uzoefu mkubwa katika teknolojia ya habari na mawasiliano.

Mwaka 2003 hadi 2004 alihudumu kama Meneja wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika Nyanza Bottling Company Ltd, ambapo alisimamia mifumo yote ya TEHAMA ya kampuni.

Katika kipindi hicho alifanikiwa kuboresha seva, mifumo ya barua pepe na miundombinu ya mtandao. Kupitia ubunifu wake, matatizo ya kiufundi yalipungua kwa asilimia 95 kutokana na matengenezo ya mara kwa mara na usimamizi bora wa mifumo ya taarifa.

Aidha, alitoa mafunzo kwa wafanyakazi kuhusu matumizi sahihi ya mifumo ya kompyuta na usalama wa taarifa, hatua iliyoongeza ufanisi wa kazi ndani ya kampuni.

Mafanikio Katika Manunuzi na Ugavi
Katika taaluma ya manunuzi na ugavi, Dk. Sajad aliwahi kuhudumu kama Meneja wa Manunuzi ambapo alisimamia mzunguko mzima wa manunuzi ya ndani na nje ya nchi.

Kupitia mikakati yake ya manunuzi na majadiliano na wasambazaji, alipunguza gharama za kampuni kwa asilimia 25.

Pia aliweka mifumo madhubuti ya ufuatiliaji wa bidhaa, kupanga viwango vya chini vya bidhaa ghala na kuboresha makadirio ya mahitaji ya malighafi. Uwezo wake huo ulimwezesha kutunukiwa Tuzo ya Forecast kutoka Coca-Cola Swaziland.

Mafanikio Katika Masoko na Mauzo
Dk. Sajad pia ametoa mchango mkubwa katika sekta ya masoko na mauzo. Akiwa Msimamizi wa Masoko wa Nyanza Bottling Company Ltd, aliongoza kampeni mbalimbali zilizosaidia kuongeza mauzo na kuimarisha ushindani wa kampuni sokoni.

Moja ya mafanikio yake makubwa ni kuanzisha programu ya VIP Club iliyoongeza mauzo kwa zaidi ya asilimia 216. Aidha, alisimamia utekelezaji wa programu za EDS na ITMO zilizofanikisha ufanisi wa asilimia 99.36.

Kupitia uwezo wake wa kujenga mahusiano bora ya biashara, alifanikiwa kuwabadilisha mawakala 75 kutoka kuwa wauzaji wa bidhaa mchanganyiko hadi washirika rasmi wa kampuni.

Tanzania na Changamoto ya Mafuta Duniani
Katika kipindi hiki ambacho dunia inakabiliwa na changamoto za upatikanaji wa mafuta kutokana na migogoro ya Mashariki ya Kati, Dk. Sajad anaamini Tanzania ipo katika nafasi nzuri zaidi kuliko mataifa mengi.

Anasema changamoto ya mafuta ni suala la kimataifa, lakini Tanzania imeweza kuvuka kipindi hicho kwa utulivu kutokana na usimamizi mzuri wa serikali na ushirikiano wa karibu kati ya sekta binafsi na taasisi za umma.

Kwa mujibu wake, baadhi ya nchi alizotembelea hivi karibuni zimekumbwa na uhaba wa mafuta uliosababisha kupanda kwa bei za tiketi za ndege, kupunguzwa kwa safari za ndege na mgao wa nishati. Hata hivyo, Tanzania imeendelea kuwa na akiba ya kutosha ya mafuta huku bei zikiwa nafuu ukilinganisha na baadhi ya mataifa jirani.

Kiongozi Anayejali Watu
Mbali na mafanikio yake ya kitaaluma, Dk. Sajad anatambulika kama kiongozi anayejali maendeleo ya wafanyakazi wake.

Anaamini mafanikio ya taasisi yoyote yanategemea uwepo wa timu yenye mshikamano, nidhamu na uwajibikaji. Kwa miaka yote aliyohudumu katika nafasi mbalimbali za uongozi, amekuwa mstari wa mbele kujenga mazingira bora ya kazi, kutoa mafunzo na kuwapa wafanyakazi nafasi ya kukuza vipaji vyao.

Historia ya Elimu na Uongozi
Safari yake ya uongozi ilianza mapema alipokuwa Meneja wa Tawi la Aptech Learning kuanzia mwaka 2000 hadi 2002. Katika nafasi hiyo alisimamia shughuli zote za tawi ikiwemo mauzo, huduma kwa wateja na usajili wa wanafunzi.

Kitaaluma, Dk. Sajad alipata elimu yake ya sekondari katika Shule ya Sekondari Mwanza alikosoma masomo ya uchumi kati ya mwaka 1993 na 1995. Elimu yake ya msingi aliipata katika Shule ya Msingi Nyakahoja, huku pia akisoma katika Shule ya Limitless Learning.

Hitimisho
Kwa kuangalia mchango wake katika sekta ya mafuta, TEHAMA, manunuzi, masoko na usimamizi wa biashara, Dk. Sajad Habib Rai ni miongoni mwa wataalamu wa Kitanzania waliochangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya sekta binafsi na uchumi wa taifa.

Kupitia ubunifu wake katika kuboresha mifumo ya ukusanyaji kodi, kuimarisha ufanisi wa biashara na kuunga mkono juhudi za serikali, ameendelea kuwa mfano wa viongozi wanaotumia taaluma zao kuleta mabadiliko chanya kwa jamii na taifa kwa ujumla.

Zaidi ya wafugaji 200 wa Kanda ya Ziwa wamepata elimu kuhusu matumizi ya mifumo ya kidigitali katika sekta ya mifugo, iliyotolewa na kampuni ya climb Up Limited, ili kuwawezesha wafugaji kuongeza tija katika uzalishaji wa mifugo bora na kuachana na mbinu za ufugaji  ambazo zimepitwa na wakati.

Hayo yameelezwa na Afisa Masoko wa kampuni hiyo, Jackline Cosmas, Mei 31 mkoani Shinyanga wakati wa kuhitimisha Maonyesho ya Mifugo ya Kanda ya Ziwa yaliyofanyika kwa muda wa siku mbili.

Baadhi ya wafugaji waliotembelea banda la Climb Up Limited na kupata mafunzo hayo wamesema elimu waliyoipata itawasaidia kubadilisha mtazamo wao kuhusu ufugaji, kutoka katika mbinu za jadi na kuelekea ufugaji wa kisasa unaotumia teknolojia kwa ajili ya kuongeza uzalishaji na ufanisi.





 

Na Said Mwishehe,Michuzi TV

HATIMAYE Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi mahiri wa Rais Dk.Samia Suluhu Hassan imetangaza rasmi kwamba kuanzia Julai 1 mwaka huu wa 2025 nchi yetu ya Tanzania itaanza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Wakati utekelezaji huo ukitarajiwa kuanza tarehe hiyo ya Julai 1, tayari upo msingi imara wa kisera, kitaasisi na kiutekelezaji unaolenga kuharakisha mageuzi ya kiuchumi, kijamii na kiutawala kwa miongo ijayo. 

Katika kikao chake kilichofanyika Dar es Salaam hivi karibuni chini ya Mwenyekiti wake, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Tume ya Taifa ya Mipango iliidhinisha miongozo na mifumo muhimu ya kusimamia utekelezaji wa Dira 2050 pamoja na kuelekeza kuharakishwa kwa miradi mikubwa ya kimkakati itakayokuwa nguzo kuu ya ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Pamoja na kuidhinisha Mwongozo wa Kitaifa wa Mipango, Mwongozo wa Kitaifa wa Uidhinishaji wa Miradi ya Maendeleo, Mwongozo wa Kitaifa wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Miradi ya Maendeleo na Mkakati wa Mawasiliano wa Dira 2050, Tume imeweka msisitizo maalum katika utekelezaji wa miradi mikubwa ya uwekezaji inayotarajiwa kuchochea mabadiliko ya kimuundo katika uchumi wa Tanzania.


Miradi hiyo ni pamoja na Mradi wa Kuchakata Gesi Asilia kuwa Kimiminika (LNG), Mradi Unganishi wa Chuma cha Liganga na Makaa ya Mawe ya Mchuchuma, Mradi wa Kabanga Nickel pamoja na Kiwanda cha Usafishaji Kahama, na Mradi wa Magadi Soda wa Engaruka. 

Kwa pamoja, miradi hiyo inawakilisha uwekezaji wenye thamani ya zaidi ya shilingi trilioni 120, sawa na takribani dola za Marekani bilioni 47.

Miradi hiyo imeainishwa kama sehemu muhimu ya utekelezaji wa Dira 2050 kwa sababu ina uwezo wa kuvutia uwekezaji mkubwa wa ndani na nje, kuongeza ajira, kuimarisha mapato ya Serikali, kukuza mauzo ya nje, kuongeza matumizi ya teknolojia za kisasa na kuimarisha ushindani wa Tanzania katika uchumi wa kikanda na kimataifa.

Mradi wa LNG unatarajiwa kuwa kichocheo kikubwa cha ukuaji wa sekta ya nishati na mapato ya fedha za kigeni. 

Liganga na Mchuchuma vinatarajiwa kuweka msingi wa maendeleo ya viwanda kwa kuongeza uzalishaji wa chuma na nishati nchini. Kabanga Nickel inaipa Tanzania nafasi ya kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kijani unaochochewa na ongezeko la mahitaji ya madini muhimu kwa utengenezaji wa betri na teknolojia za nishati safi duniani. 


Nayo Engaruka inafungua fursa mpya katika sekta ya kemikali na viwanda vinavyotegemea malighafi za ndani.

Kwa kuzingatia malengo ya Dira 2050 ya kufikia uchumi wa takribani dola trilioni moja, miradi hiyo siyo uwekezaji wa kawaida bali ni injini za mageuzi ya kiuchumi. 

Hivyo uamuzi wa Tume ya Taifa ya Mipango wa kuipa kipaumbele utekelezaji wake unaashiria dhamira ya Serikali ya kuhakikisha Dira 2050 inatafsiriwa katika matokeo halisi yatakayoongeza tija, ajira, ustawi wa wananchi na ushindani wa Taifa katika miaka ijayo.

Pamoja na hayo ukweli ni kwamba kuanza kwa utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inaonesha dhamira,kiu na shauku ya Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kuona nchi yetu inapiga hatua zaidi katika kuleta maendeleo, kuboresha hali za maisha ya wananchi na kubwa zaidi kuifanya Tanzania kuwa injini ya kukuza uchumi wake kupitia rasilimali zake .

Unapoiangalia Dira ya Taifa ya Maendeleo unaiona Tanzania tuitakayo na safari ya kuelekea huko inaanza sasa. Hongera Serikali ya Awamu ya Sita kwa hatua hii inayowasha taa ya kijani yenye matumaini makubwa kwa Watanzania.

Lakini kwa muda mrefu Watanzania tumekuwa tukiitamani Tanzania itakayokuwa na uwezo mkubwa wa kuajiri watu wake kupitia sekta mbalimbali na katika Dira hiyo imeeleza kwa kina namna ambavyo nchi inavyokwenda kuimarisha sekta hizo kama mkakati wa kutengeneza fursa za ajira kwa Watanzania.

Kwa mfano Tume ya Taifa ya Mipango chini ya Rais Dk.Samia Suluhu Hassan katika kikao chake cha Mei 26 pamoja na mambo mengine pia imeidhinisha sekta za kipaumbele 12 wakati wa utekelezaji wa dira hiyo.

Sekta hizo ni ya kilimo idadi ya viashiria vya upimaji katika mabano ni (15), viwanda na ujenzi (10), Madini na Nishati(10), Utalii(5), michezo na Sanaa(9), sekta ya ubunifu na maudhui ya kidigitali(2) wakati sekta ya miliki ,aridhi na maendeleo ya miji(13)

Pia sekta nyingine ni biashara na uwekezaji(12), Elimu(54), hifadhi za jamii,kazi na ustawi wa jamii(34), uchumi wa bluu(18) pamoja na sekta ya Sayansi,teknolojia,ubunifu na uchumi wa digitali(24).

Unapoangalia sekta hizo ambazo zimepewa kipaumbele katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 utabaini mkakati uliopo kama nchi ni kuhakikisha Tanzania inaendelea kufungua fursa zaidi ambazo kila mmoja atashiriki katika shughuli za kiuchumi na hatimaye kwa pamoja kubadilisha maisha yetu kutoka tuliyonayo sasa na kuwa na maisha bora zaidi.

Na kwa kuwa dira hiyo imelenga kubadilisha maisha yetu ni matumaini yangu wananchi wote na wa rika na kada zote tunaowajibu wa kuungana na Rais Dk.Samia na Serikali anayoiongoza katika kuwa sehemu ya safari ya kutekeleza dira hiyo ambayo ikifanikiwa kizazi kilichopo sasa na kijacho kitakuwa kwenye ile nchi ya ahadi ya asali na maziwa.

Kupitia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inaonesha jinsi ambavyo inakwenda kuinua uchumi wa mtu mmoja mmoja na lengo ni kuwezesha pamoja na kuwa na ukuaji wa uchumi kwa ujumla kama Taifa lakini pia uchumi wa kila mmoja wetu nao ukue.Ndio mpango uliopo.

Binafsi sina shaka na Rais Dk.Samia katika kusimamia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwani kwa dhamira yake na utashi wake ndio aliyetoa maelekezo ya kuandikwa kwa Dira hiyo kazi ambayo ilifanyika kwa weledi mkubwa na kupita katika hatua mbalimbali na hatimaye sasa utekelezaji wake unakwenda kuanza rasmi.

Hata hivyo nitoe rai kwa Vyama vya siasa nao wanapaswa kuwa sehemu ya kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa dira hiyo.Ni matumaini yangu kama ilivyo kwa CCM Ilani yake imeakisi kwa kiasi kikubwa yaliyomo katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Hivyo kwa vyama vya siasa vya upinzani kuakisi yaliyomo katika Dira hiyo kupitia Ilani zao.Lakini kwa kuwa utekelezaji wa dira unaanza Julai 1,2026 ni vema wanasiasa wetu bila kujali itikadi ya vyama wakaungana na Watanzania wote kuitekeleza dira hiyo.


Simu 0713833822


Mwisho



 

Kamati ya Kudumu ya Bunge inayosimamia masuala ya Utawala, Katiba na Sheria imeeleza kuridhishwa na hatua zilizofikiwa katika utekelezaji wa miradi ya uwekezaji ndani ya Eneo Maalum la Kiuchumi la Bagamoyo – BEMC. Kauli hiyo imetolewa baada ya kamati kufanya ziara ya ukaguzi ili kujionea maendeleo ya shughuli mbalimbali zinazosimamiwa na Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania, TISEZA.

Eneo la BEMC lilianzishwa kisheria kupitia Tangazo la Serikali Na. 123 la tarehe 24 Mei 2013. Lina jumla ya hekta 9,800, ambapo hekta 887 zimetengwa mahsusi kwa ajili ya Bandari ya kisasa ya Mbegani. Sehemu iliyobaki, yenye hekta 8,903, inatumiwa kwa shughuli za uwekezaji. Mradi huu unatajwa kuwa wa kimkakati kitaifa na unalenga kukuza sekta ya viwanda, biashara na uchumi kwa ujumla.

Katika Mpango wa Maendeleo wa Taifa, BEMC umetambuliwa kama moja ya nguzo zitakazosaidia Tanzania kufikia lengo la kuwa na uchumi wenye thamani ya dola trilioni moja ifikapo 2050. Kufikia Mei 2026, wawekezaji 24 tayari walikuwa wameshapatiwa maeneo na kuanza utekelezaji wa miradi yao. Miradi hiyo ipo katika hatua tofauti kama ujenzi wa viwanda, mabanda ya uzalishaji, uzio pamoja na miundombinu wezeshi.

Wakati wa ziara hiyo, Kamati ilisema imefurahishwa na kasi ya ujenzi na uwekezaji unaoendelea. Miongoni mwa miradi iliyotajwa kuvutia ni kiwanda cha Sinovest Industry Investment Limited kitakachozalisha nguo na bidhaa za nguo. Kiwanda hicho kimejengwa kwenye eneo la mita za mraba 210,080, sawa na hekta 21. Mpaka Mei 2026, uwekezaji uliofanyika ulifikia dola milioni 7 za Marekani, sawa na zaidi ya shilingi bilioni 21. Kinatarajiwa kuanza uzalishaji rasmi mwishoni mwa Juni 2026.

Kukamilika kwa kiwanda hicho kutaleta ajira nyingi. Awamu ya kwanza itazalisha ajira 1,000 za moja kwa moja, na awamu ya pili itaongeza ajira 500. Kiwanda kitatumia mashine za kisasa kuzalisha nguo zenye ubora wa kimataifa kwa ajili ya masoko ya Marekani na Ulaya.

Uwekezaji wa aina hiyo unachangia kwa kiasi kikubwa pato la Taifa, unaongeza thamani ya bidhaa za viwandani, pamoja na kuboresha kipato cha wananchi wa Bagamoyo, Mkoa wa Pwani na Tanzania nzima.

TISEZA inalenga kuhakikisha maeneo yote maalum ya uwekezaji yanatumika kikamilifu ili kuvutia mitaji na kuleta tija kwa wananchi. Lengo ni kuwafanya Watanzania wanufaike na fursa za uwekezaji katika sekta mbalimbali. Uwekezaji unabaki kuwa chombo muhimu cha kutoa ajira, kuvutia mitaji kutoka nje, kuhamisha teknolojia na kuimarisha msingi wa viwanda nchini.

Maendeleo yanayoonekana BEMC yanaonyesha nia ya dhati ya Serikali katika kuboresha mazingira ya uwekezaji na kusukuma utekelezaji wa miradi mikubwa yenye maslahi mapana kwa wananchi na Taifa.







-Pia yabainisha mkakati wa mageuzi katika mifumo ya utawala na utumishi wa umma

-Utekelezaji Dira 2050 kuanza kutekelezwa rasmi kuanzia Julai 1, 2026


Na Said Mwishehe,Michuzi TV


TUME ya Mipango ya Taifa imeidhinisha miongozo minne itakayotumika katika kusimamia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 utakaoanza Julai 1 mwaka 2026.

Akizungumza leo Mei 31 katika mkutano wa waandishi wa habari uliofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam,Waziri wa Mipango na Uewekezaji Profesa Kitila Mkumbo amesema miongozo hiyo imetolewa baada ya Tume ya Taifa ya Mipango chini ya Mwenyekiti wake Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kufanya kikao Mei 26 mwaka huu.

“Katika kikao hicho, pamoja na mambo mengine, Tume ya Taifa ya Mipango ilijadili na kuidhinisha miongozo/mikakati minne itakayotumika katika kusimamia tekelezaji wa Dira 2050 utakaonza Julai 1, 2026.”

Profesa Mkumbo ameitaja miongozo hiyo ni Mwongozo wa Kitaifa wa Mipango,Mwongozo wa Kitaifa wa Uidhinishaji wa Miradi ya Maendeleo, Mwongozo wa Kitaifa wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Miradi ya Maendeleo,Mkakati wa Mawasiliano wa Dira 2050 wa Miaka Mitano 2026/27 - 2030/31.

“Ilipojadili Muongozo wa Kitaifa wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Miradi ya Maendeleo, Tume ya Taifa ya Mipango iliidhinisha maeneo makubwa matatu ya kimkakati yanayohitaji mageuzi yenye viashiria vya upimaji 142.

“Maeneo haya na idadi ya viashiria vyake ya upimaji ni Mageuzi katika mifumo ya utawala na utumishi wa umma (Governance and civil service reforms, viashiria 13), Mageuzi katika uwekezaji na uzalishaji (structural transformation for investment, infusion and productivity, viashiria 53) pamoja na Mageuzi katika maendeleo ya kijamii, kiuchumi na mazingira (socio economic outcomes, viashiria 76)

Ameongeza pia Tume ya TaĆ­fa ya Mipango ilidhinisha sekta za kipaumbele 12 kama zilivyainishiwa katika Mpango wa Nne wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka
Mitano yenye viashiria vya upimaji 206

Amefafanua katika sekta ya kilimo idadi ya viashiria vya upimaji katika mabano ni 15, viwanda na ujenzi (10), Madini na Nishati(10), Utalii(5), michezo na Sanaa(9), sekta ya ubunifu na maudhui ya kidigitali(2) wakati sekta ya miliki ,aridhi na maendeleo ya miji(13)

Pia katika sekta ya biashara na uwekezaji(12), Elimu(54), hifadhi za jamii,kazi na ustawi wa jamii(34), uchumi wa bluu(18) pamoja na sekta ya Sayansi,teknolojia,ubunifu na uchumi wa digitali(24).

Akieleza zaidi Profesa Mkumbo ameeleza pia Tume ya Taifa ya Mipango ilielekeza kuwa Sekretariati ya Tume ijielekeze na kujikita katika kusimamia utekelezaji wa mipango ya maendeleo.

Aidha, katika kumarisha simamizi wa utekelezaji wa mipango ya maendeleo, Mwenyekiti
wa Tume alielekeza kuwa, wakati ambapo Tume haikutani katika vikao vya kawaida chini yake, wajumbe wa Tume watajigeuza kuwa Ofisi ya Usimamizi wa Utekelezaji wa Mipango (Delivery Bureau) na vikao vyake vitasimamiwa na
Makamu Mwenyekiti wa Tume.

Ameongeza Tume ya Taifa ya Mipango ilielekeza kukamilishwa kwa haraka kwa majadiliano kati ya Serikali na wawekezaji kuhusu miradi ya kimkakati ya uwekezaji inayotarajiwa kujenga msingi ya kukuza uchumi na kuchochea ajira kama sehemu muhimu ya utekelezaji wa Dira 2050 na Mpango wa Nne wa Taifa wa Maendeleo ya Miaka Mitano (2026/27 - 2030/31).

Amitaja miradi hiyo ni Mradi unganishi wa chuma cha Liganga na makaa ya mawe ya Mchuchuma, Mradi wa magadi soda wa Engaruka, Mradi wa kuchakata gesi asilia kuwa kimiminika (LNG), Mradi wa nikeli wa Kabanga (Kabanga Nickel Project) na kiwanda cha usafishaji cha Kahama.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Mhe. Profesa Kitila Alexander Mkumbo akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu kuanza Utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 (DIRA2050), tarehe 31 Mei, 2026 Ikulu, Dar es Salaam.


Top News