Waziri wa Fedha na Mipango, Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) akiwa kwenye picha ya pamoja na wenyeviti wa Bodi na Wakurugenzi wa Mashirika na makampuni ambayo serikali ina hisa chache kwenye mkutano wa mwaka 2026 uliyofanyika jijini Arusha , waliosimama wa kwanza kulia , ni Meneja Mkazi wa Barrick nchini , Dkt. Melkiory Ngido

Waziri wa Fedha na Mipango, Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) akiwa kwenye picha ya pamoja na wenyeviti wa Bodi na Wakurugenzi wa Mashirika na makampuni ambayo serikali ina hisa chache kwenye mkutano wa mwaka 2026 uliyofanyika jijini Arusha , waliosimama wa kwanza kulia , ni Meneja Mkazi wa Barrick nchini , Dkt. Melkiory Ngido.

Waziri wa Fedha na Mipango, Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) kwenye mkutano huo.

Sehemu ya washiriki wa mkutano huo.

Sehemu ya washiriki wa mkutano huo.


**
Serikali imeendelea kutambua mafanikio yanayoendelea kupatikana kutokana na ubia baina ya kampuni ya Barrick na Serikali ya Tanzania kupitia kampuni ya Twiga ambapo katika mkutano wa Wakurugenzi wenye Hisa chache za Serikali (MIF 2026) uliomalizika jijini Arusha imetunukiwa tuzo ya mshindi katika kipengele cha uwakilishi bora wa Bodi za Wakurugenzi (MIF) Directors Forum 2026 Outstanding Board Representation) na ofisi ya Msajili wa Hazina.

Barrick -Twiga imekuwa kinara wa kuendesha shughuli zake kwa kufuata sheria za madini , kanuni za nchi na kwa uwazi ambapo imefanikisha kuendesha shughuli za uchimbaji wa madini nchini kwa mafanikio sambamba na kuweza kuchangia Pato la Taifa na kunufaisha wananchi kupitia miradi mbalimbali ya kijamii inayotekelezwa kupitia migodi yake ya North Mara,Bulyanhulu na Buzwagi ambao uko katika mchakato wa kufungwa.

Mkutano huo uliowakutanisha wakurugenzi wa Bodi,Watendaji Wakuu,Watunga sera na wataalamu mbalimbali ulikuwa jukwaa la kujadili changamoto za uendeshaji na kuweka mikakati ya kuboresha utendaji wa kampuni ambazo Serikali ina hisa chache.

Katika mkutano huo ,Meneja Mkazi wa Barrick nchini,Dkt. Melkiory Ngido, alifanya wasilisho kuhusu kufikiri upya uendeshaji wa shughuli za madini kwa manufaa katika kipindi hiki cha mpito cha kimkakati katika sekta ya madini sambamba na kuwa na mifumo imara inayoweza kutekelezeka katika siku za usoni na inayoweza kusimamiwa kwa ufasaha na viongozi wa bodi.

Katika kipengele cha mabadiliko katika mazingira ya uchimbaji madini nchini aligusia masuala mbalimbali ya kuangalia kwa umakini kama vile mahitaji, siasa za kijiografia, umakini katika hatua mbalimbali kwenye tasnia kama vile kwenye uchimbaji na usindikaji na bei tete za bidhaa.

Pia aligusia masuala ya mnyororo wa thamani, kuongeza mauzo ya nje ,udhibiti wa biashara, kukidhi matarajio ya jamii kunufaika na shughuli za madini na kukidhi mahitaji ya wawekezaji.

Kuhusu suala la kufikiri upya undeshaji wa shughuli za madini kwa manufaa aligusia masuala ya athari zinazoweza kujitokeza katika uwekezaji katika tasnia ya madini nchini ikiwemo kubadilisha kanuni, kukithiri kwa uanaharakati, upotoshaji wa taarifa, siasa za kikanda na masuala endelevu.

Dkt. Ngido aligusia suala la kuimarisha mifumo kama vile kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi, huduma za maji na umeme,huduma za kimtandao ,kukuza mnyororo wa thamani wa kimataifa, teknolojia na umuhimu wa kuwa na uongozi unaotoa maamuzi kwa haraka ,kuchochea ukuaji, kujenga uaminifu na kutatua matatizo kwa haraka.

Alisema katika uendeshaji wa shughuli za madini kwa weredi baadhi ya mambo yanayopaswa kuzingatiwa aliyataja kuwa ni utekelezaji wa malengo Endelevu ya Umoja wa Mataifa, kushirikiana na wadau wa nje wenye utaalamu zaidi, kushirikisha jamii, kuweka wazi mgawanyo wa mapato, kuimarisha miundombinu, huduma za umeme na jinsi ya kurithishana ujuzi na kujenga kizazi cha wataalamu wa siku zijazo.

Kuhusu matarajio ya baadaye yanayopaswa kutazamwa katika uboreshaji wa sekta ya madini Dkt. Ngido alisema ni sera, kanuni, sheria masharti ya kutoa leseni , maslahi ya taifa, kuaminiana na kuwa na mawasiliano mazuri na taratibu nzuri za utatuzi wa migogoro.

Akihitimisha wasilisho lake katika mkutano huo, Dkt. Ngido alisema kuna umuhimu wa kuwa na mifumo katika migodi kwa njia ya uwazi,nidhamu na ushirikiano thabiti na mifumo hiyo isiwekwe kwa njia ya dharura.

Akiongea katika mkutano huo,Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu alisema ofisi yake itaendelea kuhakikisha kampuni ambazo Serikali ina hisa chache zinaendeshwa kwa ufanisi, zinatoa faida endelevu na zinachangia kikamilifu katika ajenda ya maendeleo ya muda mrefu ya nchi.


Na John Mapepele

Waziri wa Afya, Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa amesema Tanzania leo, Machi 24, 2026 imeungana na mataifa mengine duniani kuadhimisha Siku ya Kifua Kikuu Duniani, siku maalum inayolenga kuongeza jitihada za kupambana na ugonjwa huu hatari unaoendelea kuathiri mamilioni ya watu duniani.

Amewataka watanzania kuendelea kushirikiana na Serikali ili kutokomeza ugonjwa huo hapa nchini.

"Ili kuhakikisha tunafanikiwa kutokomeza ugonjwa huu, jitihada za pamoja za wadau wote katika kuwajibika zinahitajika." Amesisitiza Mhe. Mchengerwa

Aidha, katika tamko rasmi lililotolewa na Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Grace Magembe, Serikali imesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa pamoja katika kufanikisha azma ya kutokomeza kifua kikuu ifikapo mwaka 2030.

Kauli mbiu ya mwaka huu, “Kwa Jitihada za Pamoja za Viongozi, Wadau na Wananchi, inawezekana Kutokomeza Kifua Kikuu nchini,” imebeba ujumbe mzito wa uwajibikaji kwa kila mmoja.

Kauli hii inalenga kuwakumbusha viongozi, wadau wa maendeleo pamoja na wananchi kuwa mapambano dhidi ya kifua kikuu yanahitaji mshikamano na mchango wa pamoja, ikiwemo uwekezaji wa rasilimali kutoka ndani ya nchi.

Licha ya ugonjwa huu kubaki kuwa miongoni mwa magonjwa hatari ya kuambukiza, Tanzania imepiga hatua kubwa katika kupunguza maambukizi mapya.

Kwa mujibu wa takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) za mwaka 2024, visa vya kifua kikuu vimepungua kwa asilimia 44—kutoka wagonjwa 306 kwa kila watu 100,000 mwaka 2015 hadi 172 kwa mwaka 2024. 

Aidha, vifo vinavyotokana na ugonjwa huo vimepungua kwa asilimia 59, kutoka vifo 56,000 hadi 23,500 katika kipindi hicho.

Mafanikio haya yanachangiwa na uwekezaji wa Serikali katika sekta ya afya, hasa kuboresha miundombinu ya uchunguzi na upatikanaji wa dawa.

Serikali pia imehakikisha wagonjwa wanapatiwa matibabu bila malipo na kufuatiliwa ili kuhakikisha wanamaliza dozi, hatua muhimu katika kuzuia usugu wa dawa.

Hata hivyo, pamoja na mafanikio hayo, bado juhudi zinahitajika ili kufikia lengo la kutokomeza ugonjwa huu ifikapo mwaka 2035.

Serikali imeendelea kuhamasisha wananchi kujitokeza kupima mapema wanapopata dalili kama kikohozi cha muda mrefu, homa za mara kwa mara, jasho la usiku au kupungua uzito.

Aidha, jamii imetakiwa kuondoa unyanyapaa dhidi ya wagonjwa wa kifua kikuu na badala yake kuwapa msaada wa kijamii na kisaikolojia. 



Dkt. Magembe amesisitiza kuwa mgonjwa anapoanza matibabu hupunguza uwezekano wa kuambukiza wengine, hivyo ushirikiano wa jamii ni muhimu katika kudhibiti maambukizi.

Katika kukabiliana na ugonjwa huu, wananchi pia wanahimizwa kuzingatia tahadhari kama kuepuka msongamano usio wa lazima, kuhakikisha maeneo yenye hewa safi na kutoa taarifa mapema kwa wahudumu wa afya kuhusu watu wenye dalili.

Serikali, chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imeahidi kuendelea kuboresha huduma za afya hadi ngazi ya jamii ili kuhakikisha kila mwananchi anapata huduma bora kwa wakati.

Serikali inatoa wito kwa Watanzania wote kuchukua hatua ambapo kwa kufanya hivyo kutasaidia kutokomeza kifua kikuu na kulinda afya ya vizazi vya sasa na vijavyo.
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

BARAZA la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam pamoja na wadau wa mazingira, linatarajia kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Kupunguza Taka “Taka Sifuri” kwa kutoa elimu kwa wananchi juu ya mbinu za kubadilisha taka kuwa malighafi au bidhaa nyingine, hatua inayolenga kuifanya taka kuwa fursa ya kiuchumi.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Machi 24, 2026, Meneja wa Uzingatiaji wa Sheria wa NEMC, Hamadi Kissiwa, amesema maadhimisho hayo yatafanyika kuanzia Machi 28 hadi Machi 30, 2026 katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam.

Amesema kaulimbiu ya kimataifa ya maadhimisho hayo ni “Wezesha taka sifuri kwenye sekta ya chakula”, huku kaulimbiu ya kitaifa ikiwa ni “Taka ni Fursa”. Ameongeza kuwa mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Hamad Masauni.

Kissiwa amefafanua kuwa lengo kuu la maadhimisho hayo ni kubadilisha mtazamo wa jamii kuhusu taka, kwa kuhamasisha matumizi ya dhana ya 3Rs ambayo ni Kupunguza (Reduce), Kutumia tena (Reuse) na Kurejeleza (Recycle), ili kuongeza ufanisi katika matumizi ya rasilimali na kupunguza uchafuzi wa mazingira.

Amesema matumizi ya mbinu hizo yatasaidia kupunguza kiwango cha taka kinachotupwa ovyo, huku yakichangia upatikanaji wa malighafi kwa ajili ya uzalishaji wa bidhaa nyingine, hali itakayosaidia kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.

Aidha, ameeleza kuwa maadhimisho hayo pia yanalenga kuangazia changamoto ya upotevu wa chakula duniani, ambapo takwimu zinaonesha kuwa utupaji wa chakula unachangia takribani asilimia 10 ya uzalishaji wa hewa chafuzi, hali inayochangia mabadiliko ya tabianchi na kuathiri ustawi wa jamii.

Mbali na hilo, Kissiwa amewakaribisha wananchi na wadau wa mazingira kushiriki kikamilifu katika maadhimisho hayo yatakayofanyika kuanzia saa 12 asubuhi hadi saa 11 jioni, yakijumuisha maonesho ya fursa za uwekezaji katika sekta ya usimamizi wa taka pamoja na ubunifu wa bidhaa zitokanazo na taka.

Amesisitiza kuwa ushiriki wa wananchi ni muhimu katika kufanikisha ajenda ya “taka sifuri”, ambayo inalenga kujenga jamii inayotambua thamani ya taka na kuzitumia kama rasilimali badala ya kuziona kama uchafu.









Mrajis wa Vyama vya Ushirika, Dkt. Benson Ndiege amevitaka Vyama vya Ushirika vya Mazao nchini kutumia mizani za kidigitali katika kupima mazao ya wakulima ili kuondoa udanganyifu na kumlinda mkulima.


Mrajis ametoa maelekezo hayo kupitia barua ya tarehe 13 Machi, 2026 aliyowaandikia Wenyeviti na Wajumbe wa Bodi wa Vyama vya Ushirika vya mazao Tanzania Bara kuhakikisha kuwa vinatumia mizani za kidigitali kwa lengo la kuondoa udanganyifu kwenye upimaji wa mazao ya wakulima na kurahisisha upatikanaji wa takwimu sahihi za makusanyo/mauzo ya mazao.

Vyama vya Ushirika wa Mazao vitakavyobainika kuwa na Mizani ya kidijitali na havitumii Mizani hizo au kuzitumia kwa matumizi tofauti na malengo yaliyokusudiwa, vitachukuliwa hatua kwa mujibu wa Sheria; na wakulima wanatakiwa kuhakikisha mazao yao yanapimwa kwa kutumia Mizani zilizounganishwa na Mfumo wa Usimamizi wa Vyama vya Ushirika (MUVU) ili kuwawezesha kupata malipo stahiki ya mazao yao.

Aidha, Dkt. Ndiege amevitaka Vyama vyote vya Ushirika wa Mazao ambavyo bado havijatekeleza maelekezo ya ununuzi wa Mizani za kidijitali kuhakikisha kuwa vinanunua Mizani hizo kwa kufuata utaratibu wa manunuzi na Mwongozo wa Ofisi ya Mrajis kuhusu Ununuzi wa Mizani hadi kufikia Juni 31, 2026.

Tume ya Maendeleo ya Ushirika inaendelea na jitihada za kuimarisha Usimamizi wa Vyama vya Ushirika nchini ambapo kwa sasa moja ya kipaumbele kinachotiliwa mkazo ni kuratibu na kuhimiza Vyama vya Ushirika vya Mazao, kuweka utaratibu wa ununuzi wa Mizani za Kidijitali sambamba na matumizi sahihi ya mizani hizo.

MFUMO wa stakabadhi ghala umetajwa kuboresha masoko ya mazao kwa wakulima na kuwafanya kupata tija na kutambuliwa na taasisi za kifedha zinawawezesha kupata mikopo mbalimbali.

Mfumo huo umeweza kuwasaidia wakulima kutolanguliwa mazao yao na watu wa kati ‘madalali wa mazao na kupelekea wakulima kupata tija ya mazao yao.

Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB), Asangye Bangu, amesema kuwa mfumo huu umeimarika “mfumo sasa umeimarika tunatekeleza kwenye mikoa 23 kati ya mikoa 26 ya Tanzania bara na tuna bidhaa 18 zinazopita kwenye mfumo huu tija sasa inaonekana waziwazi”

Amesema kuwa tija hiyo inaonekana kwa wazalishaji mali yaani wakulima na kwa Halmashauri katika kukusanya tozo zao.

Amesema kuwa Mfumo unafanya ukusanyaki kupitia vyama vya ushirika, wakusanyaji wengine ni wafanyabiashara wenye leseni za kufanya biashara huko nyuma walikuwa wanatambulika kama madalali lakini sasa wananuzi hawa wananunua kwa bei ya sokoni kwa kuwa zinatolewa kwa uwazi.

Amesema kuwa mazoa hayo yakiingizwa gharamani huwekwa kwenye kazidata ya bodi ya stakabadhi ghalani, “kazidata hiyo ndio inayotumika na wenzetu wa soko la bidhaa na ukizungumza na sisi basi lazima uzungumze na pacha wetu muuzaji soko la bidhaa Tanzania, wao wanauza mazoa yao kidigitali na kusema kweli tumefaidika na tumeona umuhimu wa kutumia mfumo huu tukishirikiana na wamiliki wa mazao kama mazao yenye bodi basi tunashirikiana na bodi hizo lakini kwa yale mazao yasiyokuwa na bodi basi sisi tunashirikiana na Mamlaka ya udhibiti wa nafaka na mazao mchanganyiko”.

“Kwa umoja wetu tunaweza kuhakikisha mkulima yule na lile zao lake alililolitolea jasho anakwenda sokoni akirejea na tija zaidi,”alisema Bangu.

Bangu amesema kuwa tayari zao la korosho kupitia mfumo huo kwa limeuzwa kiasi cha zaidi ya tani 400,000. Na Mbaazi zaidi ya tani 200,000, ufuta tani 200,000, na sasa zao la Choroko linaendelea kuuzwa ambapo kwa sasa zishauzwa tani 60,000, .

“Unaweza kuona hata yale mazoa hayakuwahi kutegemewa kama mazoa ya kibishara sasa yanakuza uchumi wa mkulima,”amesema Bangu.

Amesema sasa wakulima wamekuwa wanatambulika na taasisi za kifedha jambo ambalo linamewahahakikisha kupata mikopo, “kimsingi tumerasmisha biashara ya mazoa”.

Bangu amesema kuwa mfumo huo unatoa ajira “kwenye kila ghala ukitoa mmiliki wa ghala kunakuwa na wafanyakazi watano pale nimekuwa nikishuhudia vijana wanaomaliza vyuo vikuu na kuja kujiunga na sekta ikiongezeka,”.

Amesema kuwa mfumo huo upo kwenye mikoa hiyo 23 na kuwashauri wakulima wote kupitisha mazao yao kwenye mfumo huo .

Bangu amesema kuwa bodi hiyo inaendelea kuwekeza kwenye maghala ya ndani na kuziingiza kwenye mifumo maghala mapya ikiwa pamoja na kuhakikisha kuwa soko la ndani linaendelea kuleta tija.

Amesema kuwa jukumu la kudhibiti ubora wa bidhaa na mazao bodi hiyo imelikabidhi kwa msimamizi wa ghala ambaye anajukumu la kuhakikisha kuwa hakuna bidhaa au zao litakaloingia likiwa halina ubora naye atahakikisha mnunuzi naye anachukua bidhaa yenye ubora.

Amesema kuwa wakulima hawalazimishwi kuuza mazao yao kwa mfumo wa stakabadhi ghalani lakini kwa yale mazao yenye bodi ni lazima mazao hayo yaratibiwe na bodi husika.

Amewakaribisha wadau mbalimbali wa kilimo na stakabadhi ghalani kwenye maadhimisho ya miaka 20 ya kuanzishwa kwa mfumo huo ambapo kutakuwa na maonesho katika ukumbi wa Jakaya Kikwete jijini Dodoma kuanzia tarehe 28 mpaka 30 Aprili mwaka huu.

Akielezea kuanzishwa kwa mfumo huo amesema kuwa ulianzishwa baada ya kubainika kuwa hiyo ndio njia itakayomaliza changamoto za soko kwa wakulima na kuhakikisha kilimo kinakuwa kina tija.

“Kimsingi mfumo huu ulianza kufanyiwa utafiti tangu 2000 ulipoonekana unaweza kuwasaidia wakulima na wazalishaji mbali maana ulionekana unaweza kufanya kazi kwa wakulima na pia kwa wazalishaji wengine ambao sio wakulima.

“Katika kuliona jambo hili na faida yake basi mwaka 2006 ikanzisha bodi ambapo sheria ilitungwa 2005 na kanuni ziliaanza 2006 na taasisi ikaanza kipindi hicho hicho kuanzia hapo mfumo ukaanza katika hatua tofauti tofauti kama mtoto kuna nyakati za kutembea, kusimama na kukimbia anavyokuwa na niwashukuuru Watanzania kwa kuendelea kuonesha nia ya kuutumia mfumo huo.

Kwa upande wake David Sukali, Mkuu wa kitengo cha Manunuzi bodi ya usimamazi wa Stakabadhi za ghala, amesema kupitia mfumo huo umewawezesha wakulima kupata mikopo na nafuu zote za kifedha.

Akizungumzia manufaa ya mfumo huo Sukali amesema kuwa “Mfumo huu unamanufaa makubwa unapotumika hususani katika mazao tukiinza na zao la korosho mathalan kwenye bei na wanunuzi kupata uhakika wa mazao,

Mbali na hilo amesema kuwa mfumo huo umewezesha wakulima kuwa karibu na soko na hivyo kurahisha kuuza mazoa kwa bei yenye tija na kwa haraka,
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi ghala (WRRB) Asangye Bangu



Mwenyezi Mungu akitaka jambo litokee  hutokea ndivyo ilivyotokea, uumbwaji wa Kasoko ya Ngorongoro zaidi ya miaka milioni 2.5 iliyopita ambapo mlima mrefu uligeuzwa kuwa bonde la Ngorongoro.

Wanafunzi wa madrasa kutoka jimbo la Kondoa mkoani Dodoma pamoja na walimu wao wameshuhudia uwezo huo wa Mwenyezi Mungu walipotembelea hifadhi ya Ngorongoro katika ziara iliyoandaliwa na mbunge wa jimbo hilo mheshimiwa Dkt Ashatu Kijaji (Mb)

Afisa Mhifadhi Mkuu na mkuu wa makumbusho ya Urithi Geopark Dkt. Agnes Gidna aliwaeleza wanafunzi na waalimu hao kuwa mlipuko mkubwa wa volcano uliugeuza mlima mkubwa uliokuwepo eneo hilo  zaidi ya miaka milioni 2.5 iliyopita na kuwa kreta hii ni kudhihirisha wazi kwamba kwa Mungu hakuna kubwa.

Akizungumza kwa niaba ya kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka hiyo, Kamishna Msaidizi Mwandamizi Gloria Bideberi amempongeza mbunge wa jimbo hilo Dkt. Ashatu Kijaji ambaye pia ni waziri wa maliasili na Utalii kwa kusimamia sekta hiyo kwa vitendo ambapo ujio wa wanafunzi hao utaongeza jitihada za kutangaza utalii wa ndani.

Kiongozi wa Ujumbe huo Katibu wa Idara ya Elimu ofisi ya mbunge wa jimbo la Kondoa Ayoub Sogoi amesema ziara hiyo imedhihirisha kwa vitendo mafunzo wanayopata vijana hao kutoka madrasa na shule za msingi na sekondari.









VUNJO.

MBUNGE wa Jimbo la Vunjo mkoani Kilimanjaro, Enock Koola ameendelea na ziara yake ya kuhamasisha kilimo cha kahawa katika jimbo hilo ambapo mamia ya wakulima wakijitokeza kushiriki na kupata elimu kuhusu mbinu bora za uzalishaji wa zao hilo la kimkakati.

Katika mwendelezo wa ziara hiyo, Mbunge pamoja na timu yake ilitembelea kata za Mwika Kaskazini na Mamba Kaskazini, akiambatana na Mbunge wa Viti Maalum, Dkt. Catherine Joachim pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Godfrey Mnzava kuhamasisha wakulima wa zao la kahawa.

Akizungumza na wananchi, Koola alisisitiza umuhimu wa kufufua na kuimarisha kilimo cha kahawa kama nguzo kuu ya uchumi wa wananchi wa Vunjo.

Alibainisha kuwa juhudi za pamoja kati ya serikali, viongozi wa kisiasa na wakulima ni msingi wa kuongeza uzalishaji, kuboresha ubora wa kahawa, na kuhakikisha wakulima wanapata masoko yenye tija.

Kwa upande wake, Dkt. Catherin Joachim aliwahimiza wakulima kuchangamkia fursa zilizopo katika sekta ya kahawa kwa kuzingatia ushauri wa wataalamu wa kilimo na kutumia mbinu za kisasa ili kuongeza tija na kipato.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Mnzava, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano kupitia vyama vya ushirika pamoja na matumizi sahihi ya pembejeo ili kuongeza ushindani wa kahawa ya Vunjo katika soko la ndani na kimataifa.

Wakulima wamepongeza jitihada za Mbunge kwa kushirikiana na Serikali katika kuhakikisha zao la kahawa linakuza uchumi wa kaya na maendeleo ya jamii katika eneo hili.





Na Emmanuel Mbatilo, Kibaha

Wananchi wa Kijiji cha Kitomondo, wilayani Kibaha mkoani Pwani, wameiomba Serikali kuingilia kati mgogoro wa ardhi uliodumu kwa zaidi ya miaka 20 kati yao na mfugaji anayedaiwa kumiliki eneo la takribani hekari 7,000.

Eneo hilo linaelezwa kuenea hadi wilaya jirani ya Kisarawe na kusababisha wananchi kukosa maeneo ya kutosha kwa ajili ya shughuli za maendeleo, ikiwemo kilimo.

Wananchi hao wamesema mgogoro huo umeathiri maisha yao kwa kiasi kikubwa, huku wakidai kuwa umewanyima fursa ya kujiletea maendeleo kupitia matumizi ya ardhi.

Kwa upande wao, wananchi wameisisitiza Serikali kuingilia kati haraka ili kumaliza sintofahamu iliyopo, wakieleza kuwa kuchelewa kwa suluhisho kunazidi kuathiri ustawi wa kijiji hicho.

Akizungumza kwa njia ya simu Machi 22, 2026, Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Nickson Simon, amesema tayari timu ya wataalamu imefanya uhakiki wa mipaka na kubaini kuwa chanzo kikuu cha mgogoro huo ni uuzaji holela wa ardhi.

Amesema baada ya suala hilo kufikishwa ofisini kwake, alipendekeza njia mbili za kutatua mgogoro huo, ambazo ni kufikia maridhiano kati ya pande husika au kufungua kesi katika Mahakama ya Ardhi ili kupata ufafanuzi wa kisheria.

Naye Mwenyekiti wa Kijiji cha Kitomondo, Ramadhani Kiluka, amesema kuchelewa kwa utatuzi wa mgogoro huo kunaweza kusababisha wananchi kupoteza imani kwa Serikali.

Amesema kuwa iwapo hatua za haraka hazitachukuliwa, hali hiyo inaweza kuendelea kudhoofisha maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika eneo hilo.






Serikali kupitia Tume ya Madini imeendelea kusisitiza umuhimu wa utekelezaji madhubuti wa sheria na kanuni katika sekta ya madini, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuhakikisha rasilimali za taifa zinawanufaisha Watanzania na kulinda maslahi mapana ya nchi.

Akizungumza jijini Dodoma katika kikao kazi kilichowakutanisha wawakilishi wa mawakili kutoka Wizara ya Katiba na Sheria, Ofisi ya Mwasheria Mkuu wa Serikali pamoja na viongozi kutoka Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) na taasisi ya Breakthrough Attorneys, Mkurugenzi wa Ukaguzi na Biashara ya Madini, CPA Venance Kasiki, amesema wanasheria na kampuni za sheria ni wadau muhimu katika kuimarisha ufuataji wa sheria na utatuzi wa migogoro katika sekta hiyo.

Amesema uwepo wa ushauri bora wa kisheria unachangia kuongeza ufanisi wa shughuli za uchimbaji, hususan kwa wamiliki wa leseni, wakandarasi na watoa huduma migodini, hivyo kuchochea ukuaji endelevu wa sekta ya madini.

CPA Kasiki amefafanua kuwa kikao hicho kimeandaliwa mahsusi kujenga uelewa wa pamoja kuhusu utekelezaji wa Kanuni ya 13A ya Kanuni za Ushirikishwaji wa Watanzania katika nyanja ya huduma za kisheria, akisisitiza umuhimu wa wadau hao kuzingatia weledi, uadilifu, uwazi na gharama nafuu katika utoaji wa huduma zao.

“Ni muhimu kwa kampuni za sheria na wanasheria binafsi kuhakikisha wanatoa huduma zenye viwango vya juu vya taaluma, zitakazochochea uwekezaji na kulinda maslahi ya Taifa,” amesema CPA Kasiki.

Aidha, amewataka wanasheria wa ndani kujenga uwezo wa kitaaluma ili waweze kushindana katika miradi mikubwa ya kimkakati, hususan katika kukabiliana na changamoto ya kuoanisha mikataba ya kimataifa na sheria za ndani.

Kwa upande mwingine, maboresho ya Sheria ya Madini, Sura ya 123 pamoja na kanuni zake, yameendelea kuweka mkazo katika kuongeza ushiriki wa Watanzania kupitia utoaji wa kipaumbele kwa bidhaa na huduma za ndani, ikiwemo huduma za kisheria.

Amesema utekelezaji wa Kanuni za Ushirikishwaji wa Watanzania za mwaka 2018 umeleta mafanikio makubwa, yakiwemo ongezeko la ajira, kukuza matumizi ya bidhaa na huduma za ndani, uhamishaji wa teknolojia pamoja na kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu nafasi yao katika sekta ya madini.

CPA Kasiki amebainisha kuwa wanasheria wana jukumu la msingi katika kuhakikisha mafanikio hayo yanaendelea kudumishwa, ikiwa ni pamoja na kutoa ushauri wa kisheria, kusimamia mikataba ya ubia, kuhakikisha kipaumbele kinatolewa kwa Watanzania katika ajira na huduma, pamoja na kushiriki kikamilifu katika utatuzi wa migogoro.

Kikao kazi hicho kimejadili kwa kina uwezo, mchango na mafanikio ya kampuni za sheria zinazomilikiwa kwa asilimia 100 na Watanzania, pamoja na kubaini changamoto zilizopo na kupendekeza mikakati ya kuboresha ushiriki wao katika sekta ya madini.






 

Na Mwandishi Wetu.

TANZANIA imepata uwakilishi miongoni mwa wanufaika wa Mpango wa Ujasiriamali wa Tony Elumelu Foundation (TEF) wa mwaka 2026, huku wajasiriamali 12 wakichaguliwa katika kundi la kwanza la washindi waliotangazwa barani Afrika.

Hayo yalitangazwa katika Transcorp Hilton Abuja, ambapo wajasiriamali 1,951 walibainishwa kama sehemu ya wanufaika wapatao 3,200 watakaosaidiwa na TEF mwaka huu.

Uteuzi huo ulifuatia mchakato wenye ushindani mkubwa uliovutia zaidi ya waombaji 260,000 kutoka nchi 54 za Afrika.

Kundi la mwaka 2026 litatangazwa kwa awamu ili kukuza ushirikishwaji na kupanua ushiriki wa kisekta. Kundi la kwanza linajumuisha wajasiriamali 1,951 waliochaguliwa chini ya Mpango wa Kina wa TEF.

Makundi mengine yatakayotangazwa baadaye mwaka huu ni pamoja na wajasiriamali 100 chini ya Mpango wa Kudhibiti Taka, wajasiriamali 100 chini ya Mpango wa Aguka nchini Rwanda, na wajasiriamali 1,049 chini ya Mpango wa Wanawake wa Afrika, ambapo ushiriki kutoka Tanzania unatarajiwa kuongezeka.

Kila mjasiriamali aliyechaguliwa atapokea dola 5,000 (takribani Sh12,950,000) katika ufadhili wa mbegu kama mtaji wa kuanzia, pamoja na mafunzo ya biashara, ushauri na ufikiaji wa mtandao wa Afrika nzima, unaolenga kuharakisha ukuaji wa biashara na fursa za ajira.

Kujumuishwa kwa Tanzania katika kundi hili kunaonyesha ushiriki wake unaoendelea katika mfumo wa ikolojia wa ujasiriamali Afrika, huku pia ukiangazia fursa ya kuongeza ushindani katika mizunguko ijayo ya maombi.

Barani Afrika, wanawake ni asilimia 51 ya wajasiriamali waliochaguliwa ikilinganishwa na asilimia 49 ya wanaume, jambo linaloonyesha dhamira ya TEF katika usawa wa kijinsia.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Tony Elumelu alieleza jukumu muhimu la ujasiriamali katika kuleta mabadiliko ya kiuchumi na kushughulikia ukosefu wa ajira kwa vijana barani Afrika, akisisitiza umuhimu wa kuweka mazingira rafiki kwa biashara.

Mwanzilishi mwenza Awele Vivian Elumelu aliwahimiza waombaji ambao hawakuchaguliwa kutokata tamaa, bali waendelee kutuma maombi katika mizunguko ijayo.

Mpango wa Ujasiriamali wa TEF ni miongoni mwa mipango inayoongoza barani Afrika katika kusaidia wajasiriamali kupitia ufadhili, kukuza uwezo na ushauri.

Maombi ya mzunguko unaofuata yamefunguliwa, Watanzania pamoja na Waafrika wengine wanahimizwa kutuma maombi yao kabla ya mwisho wa Machi 2026.





Na Munir Shemweta, WANMM

Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imewasilisha Randama ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya Bajeti kuu ya Serikali.

Akiwasilisha randama hiyo leo tarehe 23 Machi, 2026 jijini Dodoma, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo amesema wizara yake imejipanga kuendelea kutekeleza vipaumbele muhimu vinavyolenga kuboresha sekta ya ardhi, ikiwa ni pamoja na kuongeza kasi ya upimaji wa ardhi, utoaji wa hati miliki, pamoja na kudhibiti migogoro ya ardhi nchini.

Ameongeza kuwa, katika mwaka wa fedha 2026/2027, wizara inalenga kuimarisha mifumo ya kidijitali katika usimamizi wa ardhi ili kuongeza uwazi, ufanisi na mapato ya Serikali. Aidha, juhudi zaidi zitaelekezwa katika kupanga, kupima na kumilikisha ardhi katika maeneo ya mijini na vijijini.

Uwasilishaji wa Randama hiyo ni hatua muhimu katika mchakato wa kupitia na kuboresha Bajeti ya Wizara kabla ya kuwasilishwa rasmi bungeni kwa ajili ya kujadiliwa na kupitishwa.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akizungumza wakati wa kuwasilisha Randama ya Wizara yake kwa mwaka wa fedha 2026/2026 mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii tarehe 23 Machi 2026 jijini Dodoma. Kushoto ni Naibu Waziri wa Ardhi Mhe. Kaspar Mmuya na kulia ni Katibu Mkuu Mhandisi Anthony Sanga.
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Mhe. Timotheo Mnzava akisisitiza jambo wakati wa uwasilishwaji Randama ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa mwaka wa fedha 2026/2027 tarehe 23 Machi 2026 jijini Dodoma. Kushoto ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Mary Masanja.
Mkurugenzi wa Sera na Mipango wa Wizara wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt. Netho Ndilito akizungumza wakati wa kuwasilisha Randama ya Wizara ya Ardhi mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii tarehe 23 Machi 2026 jijini Dodoma.

Sehemu ya wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii wakifuatilia uwasilishwaji wa Randama ya Wizara ya Ardhi jijini Dodoma tarehe 23 Machi 2026. (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)



Kuelekea uzinduzi wa WazoHuru Air BnB Apartments Mtaa wa Unyankae-Miembeni Manispaa na Mkoa wa Singida, Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Wazohuru Media Group Limited amechangia vifaa vya michezo kwenye shule za msingi katika Manispaa ya Singida vyenye gharama ya shilingi Milioni 4.2

Vifaa hivyo vya michezo ni pamoja na jezi Jozi moja yenye jezi 16 na mpira mmoja katika shule ya Msingi Tumaini Viziwi, S/M Ukombozi, S/M Kindai, S/M Sumaye, S/M Mtipa na S/M Unyankae.

Pia amechangia Jozi moja yenye jezi 16 na mpira mmoja kwa timu ya Umoja wa Michezo na Taaluma Tanzania kwa Shule za Msingi (UMITASHUMTA) Manispaa ya Singida kwa ajili ya kuanza mashindano ya michezo hiyo mwaka huu 2026.

Akizungumza mara baada ya makabidhiano hayo, Mathias Canal amesema kuwa Lengo kuu la zoezi hilo ni kuhamasisha michezo mashuleni, kukuza vipaji vya wanafunzi, pamoja na kuchangia maendeleo ya afya na ustawi wa watoto.

Ameeleza kuwa pamoja na mambo mengine lakini pia kampuni yake imekabidhi vifaa hivyo vya michezo ikiwa ni sehemu ya mrejesho katika jamii baada ya kukamilika kwa ujenzi wa majengo 7 ya WazoHuru Apartments.

Mathias amebainisha kuwa tarehe 28 Machi 2026, kuanzia saa kumi na mbili kamili jioni (12:00) mradi huo wa eneo hilo la makazi ya kisasa utazinduliwa ambapo mgeni rasmi katika tukio hilo atakuwa ni Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe Halima Dendego.










Top News