Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza, Bw. Balandya Elikana,akizungumza wakati akifungua mafunzo ya kuwajengea uwezo wafanyabiashara jijini Mwanza,ili kuwaongezea uelewa kuhusu masuala ya ushindani wa soko pamoja na taratibu za kupata haki katika shughuli za kibiashara yaliyoandaliwa na Baraza la Ushindani wa Soko (FCT).
Na.Mwandishi Wetu-MWANZA
BARAZA la Ushindani wa Soko (FCT) limetoa mafunzo ya kuwajengea uwezo wafanyabiashara jijini Mwanza, yakilenga kuwaongezea uelewa kuhusu masuala ya ushindani wa soko pamoja na taratibu za kupata haki katika shughuli za kibiashara.
Mafunzo hayo yaliwakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya biashara, ambapo waliipongeza Wizara ya Viwanda na Biashara chini ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa juhudi zake za kuweka mazingira bora ya biashara na uwekezaji kupitia uwepo wa chombo huru cha kusimamia na kudhibiti ushindani wa soko.
Akifungua semina hiyo, Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza, Bw. Balandya Elikana, alisema kuwa mafunzo hayo ni muhimu kwa wadau wa sekta ya biashara kwani yanawawezesha kuelewa kwa kina majukumu ya Baraza la Ushindani pamoja na umuhimu wa mshikamano katika utekelezaji wa sheria za ushindani.
“Kupitia semina hii, wadau watapata uelewa mpana kuhusu Baraza la Ushindani na nafasi yake katika kulinda haki za mlaji pamoja na kuendeleza ushindani wa haki katika soko.”Alisema Bw.Elikana
Akizungumza katika mafunzo hayo, Msajili wa Baraza la Ushindani, Bw. Mbegu Kaskasi, alisema kuwa Baraza lipo kwa ajili ya kulinda masuala yote yanayohusu ushindani wa soko na kuchochea maendeleo ya kiuchumi nchini. Alieleza kuwa utekelezaji wa majukumu ya Baraza unalenga kuimarisha misingi ya utawala bora kwa kuhakikisha sheria za ushindani zinatekelezwa kikamilifu, kwa haki na kwa uwazi.
Aidha, aliongeza kuwa Baraza huhakikisha mamlaka za udhibiti zinazingatia taratibu na kanuni za ushindani wakati wa utekelezaji wa majukumu yao, sambamba na kutoa majibu sahihi na ya haraka katika migogoro ya kibiashara. Alibainisha kuwa hatua hiyo inalenga kumlinda mlaji dhidi ya vitendo vinavyodhoofisha ushindani, hivyo kuchangia katika ujenzi wa uchumi shindani, jumuishi na wenye tija kwa Watanzania.
Kwa upande wake, Meneja wa Mkoa wa Chemba ya Wafanyabiashara, Bw. Hassan Karambi, alisema kuwa amepata elimu yenye manufaa makubwa kupitia programu ya Baraza ya kuwajengea uwezo wadau.
Alieleza kuwa mafunzo hayo yamewasaidia wafanyabiashara kufahamu kuwa endapo hawataridhika na maamuzi ya mamlaka za udhibiti kama LATRA, TCRA, TCAA, EWURA, PURA pamoja na Tume ya Ushindani (FCC), wana haki ya kukata rufaa katika Baraza la Ushindani ili kupata haki yao.
Naye Meneja wa Mamlaka ya Mawasiliano Kanda ya Ziwa, Bi. Imelda Salumu, alifafanua utaratibu wa Baraza katika kupokea rufaa kutoka kwa wadau.
Alisema kuwa malalamiko huanza kwa mtoa huduma husika, na endapo hayatapatiwa ufumbuzi, hufikishwa katika mamlaka ya udhibiti kama hatua ya kwanza ya rufaa. Aliongeza kuwa iwapo mlalamikaji hataridhishwa na maamuzi ya mamlaka hiyo, utaratibu humruhusu kuwasilisha rufaa katika Baraza la Ushindani kwa hatua zaidi za kisheria.


SERIKALI imeanza utekelezaji wa mradi mkubwa wa kusambaza umeme katika vitongoji 267 vya Mkoa wa Manyara kwa gharama ya Shilingi bilioni 45.8 kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA), ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya umeme na kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.
Akizungumza wakati wa hafla ya kumtambulisha mkandarasi wa mradi huo, mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Herini Mhina, amesema mkataba wa utekelezaji wa mradi huo ni wa miaka mitatu na utatekelezwa katika halmashauri zote za Mkoa wa Manyara.



Mhandisi Mhina amesema mradi huo unalenga kufikisha huduma ya umeme katika vitongoji ambavyo bado havijafikiwa, hatua itakayosaidia kuboresha maisha ya wananchi, kukuza shughuli za kiuchumi pamoja na kuimarisha upatikanaji wa huduma za kijamii kama afya na elimu.


Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, amewaagiza Wakuu wa Wilaya zote za mkoa huo kutoa ushirikiano wa karibu kwa mkandarasi ili kuhakikisha mradi unatekelezwa kwa wakati na kwa viwango vinavyotakiwa.
Mhe. Sendiga pia amesisitiza umuhimu wa viongozi kutoa elimu kwa wananchi kuhusu utekelezaji wa mradi huo, akieleza kuwa mradi wa kusambaza umeme hauna fidia, hivyo ni muhimu wananchi kuelewa taratibu zake ili kuepusha changamoto zisizo za lazima.


Naye mkandarasi aliyekabidhiwa utekelezaji wa mradi huo, Bw. Patrick Mong, amesema lengo lao ni kuukamilisha mradi huo ndani ya miezi 33, huku akibainisha kuwa kazi za utekelezaji zinaanza rasmi Februari 9 mwaka huu.Amesema mkandarasi amejiandaa kikamilifu kuhakikisha mradi unakamilika kwa ubora na kwa muda uliopangwa ili wananchi wa Mkoa wa Manyara wanufaike na huduma ya umeme kwa maendeleo endelevu.
Na Kassim Nyaki, Ngorongoro.
Mabadiliko makubwa katika ushirikishwaji wadau wa sekta ya utalii yameibuliwa na uongozi Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro ikianza mwanzo wa safari mpya ya simulizi kwa chapa ya Destination Ngorongoro kwa kuzungumza sauti moja, iliyo thabiti, yenye kujiamini na kukumbukwa.
Ngorongoro imeamua kuzindua shindano la upigaji picha kwa waongoza watalii (Tour Guides) lijulikanalo kama “The Birth of Wonders photo competition” katika eneo la Ndutu hususan msimu huu wa mazalia ya Nyumbu.
Akitangaza kampeni hiyo Kamishna Msaidizi Mwandamizi anayesimamia huduma za Utalii na Masoko Mariam Kobelo ameeleza kuwa shindano hilo linahusu eneo la Ndutu ambapo ndipo Safari Kuu ya Nyumbu huzaliwa na maisha kuanza ambapo eneo hilo hadithi ya Ngorongoro hujirudia upya kila mwaka.
“Waongoza Watalii ni mabalozi wetu muhimu katika kuisimulia Ngorongoro kwa dunia, katika msimu huu wa uzaaji wa nyumbu hapa Ndutu, tunawaalika kutumia lenzi zao kunasa pumzi za kwanza za uhai wa ndama, hatua za kwanza za ndama, mahusiano ya mama na mwana,
Waongoza watalii watapaswa kupiga picha na kuzituma kupitia akaunti zao za instagram, _tag_ na kushiriki (collaborate) na akaunti rasmi ya _instagram_ ya ngorongoro ijulikanayo kama (@visitngorongoro
Katika shindano hilo la upigaji picha ( _The Birth of Wonders photo competition)_ Washindi watachaguliwa kwa kuzingatia ushiriki (engagement) wa watazamaji pamoja na kufuata masharti yote ya shindano ambapo mshindi wa kwanza atajinyakulia kitita kinono cha shilingi Milioni 3,000,000, mshindi wa pili shilingi milioni 2,000,000 na mshindi wa tatu atajishindia shilingi milioni 1,000,000 mtawalia.
Waongoza Watalii ambao ni washiriki wa kampeni hii wanakuwa wasimulizi wa sauti ya chapa ya _Destination Ngorongoro_ Kwani wao ndiyo mashuhuda wa kwanza wa simulizi ya uzao wa nyumbu.
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), amekipongeza Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA) kwa kuweka mipango na mikakati inayotembea katika maono ya dira Taifa ya mwaka 2025-2050, ikiwemo mageuzi ya Kidijitali na Utafiti na Maendeleo.
Mhe. Luswetula ameyasema hayo Februari 06, 2026 katika mahafali ya 27 ya IAA duru ya Pili, yaliyofanyika Ngurodoto jijini Arusha akimwakilisha Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Omar Mussa.
Mhe. Luswetula amesema mipango inayofanywa na IAA ya kuboresha miundombinu ya TEHAMA, mifumo ya kujifunzia kwa njia ya mtandao hususani kwa Shahada ya Uzamili (master’s degree), usimamizi wa kitaaluma ni nguzo muhimu katika kuongeza ufanisi na ushindani wa Chuo kitaifa na kimataifa.
“Mageuzi ya Kidigitali ni kichocheo muhimu cha maendeleo hususani katika kuboresha ukuaji wa uchumi na kuimarisha huduma za jamii ikiwemo elimu. Serikali inatambua na kupongeza juhudi za IAA katika kuwekeza kwenye mifumo ya kidigitali”, amesema Mhe.Luswetula.
Aidha, ameipongeza IAA kwa kuendelea kuzalisha wataalam mahiri wa fedha, uhasibu, uchumi, kodi, utalii, usimamizi biashara, benki, ununuzi na ugavi, masoko, bima, TEHAMA na nyingine nyingi; ambao wamekuwa mhimili muhimu katika ukusanyaji wa mapato ya Serikali, usimamizi wa fedha za umma, sekta binafsi, taasisi za kifedha na miradi ya maendeleo.
Vile vile, Mhe.Luswetula awasisitiza wanafunzi na wahitimu wa Shahada ya Uzamili kuimarisha zaidi tafiti zao za kitaaluma kwa kuzielekeza katika kutoa majibu ya changamoto halisi zinazoikabili jamii na Taifa letu, ikiwemo masuala ya usimamizi wa fedha za umma, ukuaji wa uchumi jumuishi, ajira, ubunifu, na matumizi sahihi ya teknolojia.
Mkuu wa Chuo IAA, Prof. Eliamani Sedoyeka amesema IAA wanajivunia kuwa miongoni mwa taasisi za elimu ya juu nchini zinazotekeleza mwelekeo wa Kitaifa wa kupanua upatikanaji wa elimu ya juu kwa kuanzisha na kuimarisha mfumo jumuishi wa utoaji wa shahada ya Uzamili (Master’s degree) unaochanganya masomo ya ana kwa ana darasani (Physical classes) na ya mtandaoni kwa wakati mmoja yaani ‘blended mode’.
Prof Sedoyeka ameongeza kuwa IAA imeweka mkakati kuwawezesha wahadhiri wengi zaidi kusomea Shahada ya Uzamivu, ili kukidhi ongezeko la idadi ya wanafunzi wa Uzamili linaloendelea kushuhudiwa kila mwaka, ambapo jumla ya wahadhiri 115 wamepelekwa kusoma Shahada ya Uzamivu (PhD) katika vyuo mbalimbali nchini na nje ya nchi katika mwaka wa masomo 2025/2026.
Naye Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo IAA, Dkt. Mwamini Tulli amesema Katika mahafali ya 27 duru hii ya pili jumla ya wahitimu 2,250 kati yao wanaume ni 1,369 sawa na asilimia 60.8 na wanawake 881 sawa na asilimia 39.2 wametunukiwa Shahada ya Uzamili ya Chuo cha Uhasibu Arusha(IAA) katika fani 15.
Wito huo umetolewa na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Rahma Kisuo, leo Februari 07, 2026 katika ukumbi wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya kuwaaga rasmi vijana 200 wanaoenda kufanya kazi nje ya nchi.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Kisuo amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuimarisha mifumo ya kisheria na kitaasisi ya kusimamia ajira nje ya nchi, kwa lengo la kuhakikisha Watanzania wanapata ajira zenye staha.
Ameeleza kuwa, Serikali imeendelea kuratibu na kusimamia shughuli za Mawakala Binafsi wa Ajira waliosajiliwa, ambao wanauganisha Watanzania na fursa za ajira nje ya nchi kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizopo.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Huduma za Ajira, Jane Sorogo, amewashukuru Mawakala Binafsi wa Ajira kwa namna wanavyoshirikiana na Serikali katika kuwaandaa vijana wanaopata fursa za ajira nje ya nchi.
Naye, Makamu Mwenyekiti wa Mawakala wa Ajira nchini, Rashid Milao, ametoa wito kwa vijana waliopata fursa hizo za ajira kuzingatia maelekezo wanaliyopewa na Serikali ili kuiwakilisha vyema Tanzania kimataifa.



Mwenyekiti wa halmashauri ya Mji Handeni, Amiri Mwaliko,akizungumza katika mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju,akizungumza katika mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.
Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Reuben Kwagilwa,akiteta jambo na Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese,wakati wa mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.

Sehemu ya Madiwani wakifuatilia mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata za Halmashauri ya Mji Handeni uliofanyika leo Februari 7, 2026.
Na Augusta Njoji
MWENYEKITI wa Halmashauri ya Mji Handeni, Mhe. Amiri Mwaliko, amempongeza Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan, kwa kutoa kibali cha ajira kilichowezesha kupatikana kwa watumishi 82 wa kada mbalimbali na hivyo kupunguza uhaba wa watumishi katika halmashauri hiyo.
Akifungua mkutano wa kupokea na kujadili taarifa za kata wa Halmashauri hiyo uliofanyika Februari 7, 2026 mjini hapa, Mhe. Mwaliko amesema serikali imeendelea kuchukua hatua za kutatua changamoto ya upungufu wa watumishi.
“Tunaishukuru serikali kwa kuendelea kutatua changamoto ya watumishi. Tunafurahia hatua hii kwa kuwa lengo la serikali ni kuondoa uhaba wa watumishi na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi,” amesema.
Aidha, amempongeza Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, kwa kuhakikisha wilaya hiyo inaendelea kudumisha amani na utulivu.
Mhe. Mwaliko amewataka viongozi na watumishi kushirikiana katika kujenga halmashauri yenye mshikamano na kutatua changamoto zinazojitokeza.
Ameongeza kuwa ni muhimu kusimama pamoja na watumishi na kushughulikia changamoto kwa njia ya mazungumzo ili kujenga timu imara ya utendaji kwa maendeleo ya halmashauri.
Kadhalika, amesisitiza kuendelea kuchukuliwa hatua za kudhibiti utoro wa wanafunzi kwa kushirikiana na madiwani wa maeneo husika.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju, amesema katika mwaka wa fedha 2025/26 serikali imeajiri watumishi 82 wakiwemo walimu wa shule za msingi na sekondari pamoja na wauguzi.
Amesema changamoto ya upungufu wa watumishi inaendelea kupatiwa ufumbuzi kadri serikali inavyoendelea kutoa ajira, huku halmashauri ikiendelea kutenga bajeti kupitia mapato ya ndani kwa ajili ya kuchangia maendeleo ya kata, ikiwemo ununuzi wa madawati.



.jpeg)

.jpeg)
















