Na Mwandishi wetu, Simanjiro
HALMSHAURI ya Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara, baada ya kupata mradi wa mpango wa kukabiliana na mabadiliko ya Tabianchi (SCALE), wataalamu mbalimbali wamekuwa wakipita maeneo tofauti yatakayonufaika na mpango huo kwa kutoa elimu kwa jamii.


Wananchi wa Kijiji cha Olchoronyori Kata ya Msitu wa Tembo, wamepatiwa elimu endelevu kuhusu mbinu za kuhimili na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi, ikiwa ni mkakati wa kujenga jamii inayostahimili majanga ya kimazingira.

Elimu hiyo imetolewa kupitia Mpango wa Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi (SCALE), kwa kipindi cha miaka mitano. Lengo likiwa ni kuwajengea wananchi uelewa wa namna ya kuzuia na kukabiliana na majanga kama vile ukame wa muda mrefu, mafuriko, milipuko ya magonjwa, pamoja na tishio la njaa.

Akizungumza katika mkutano wa wananchi uliofanyika katika kijiji hicho mwezeshaji wa mafunzo hayo mhandisi Joanes Martine amewataka wananchi kuwa mabalozi wema katika jamii zao kwa kuhakikisha wanasimamia sheria na taratibu za utunzaji wa mazingira.

“Nawasihi mkawe mabalozi katika jamii zenu. Shirikianeni kwa pamoja kufuata kanuni bora za utunzaji wa mazingira ikiwemo upandaji wa miti, kilimo endelevu, na kukomesha kabisa tabia ya ukataji miti ovyo pamoja na uchomaji mkaa,” alisisitiza mhandisi Joanes.

Pia, mwezeshaji huyo amewataka wananchi kuwa mstari wa mbele katika kuchochea maendeleo kwa kuibua miradi na fursa mpya zitakazovutia uwekezaji zaidi kutoka serikalini, hatua itakayosaidia kukuza uchumi wa jamii hiyo na taifa kwa ujumla.

Hata hivyo, mpango huo unafanyika kwa kuratibiwa na timu ya mabadiliko ya tabianchi kutoka ngazi ya Halmashauri (CCAT) kwa kushirikiana na timu ya mabadiliko ya tabianchi ngazi ya kata (WCAT).

Kata sita za Oljoro namba tano, Shambarai, Msitu wa Tembo, Loiborsoit, Ruvu Remit na Kitwai zinatarajiwa kunufaika na mradi huo wa SCALE.

Mradi huo wa SCALE unatekelezwa katika mikoa 21 ya Tanzania bara katika halmshauri 54 na mikoa mitano ya Zanzibar kwenye Halmashauri 11.


BARAZA la Madiwani la Halmashauri ya Jiji la Dodoma limewafukuza kazi watumishi watatu na mtumishi mmoja kushushwa cheo na mshahara kufuatia kukiuka misingi na taratibu za Utumishi wa Umma.

Maamuzi hayo yalifanyika katika Mkutano maalum wa Mashauri ya Kinidhamu uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Watumishi waliofukuzwa kazi ni Afisa Muuguzi Msaidizi, Muuguzi na Afisa Mtendaji wa Mtaa. Mtumishi aliyeshushwa cheo na mshahara ni Mteknolojia Maabara.

Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Alimwoni Chaula alilihoji Baraza la Madiwani, na kwa kauli moja liliridhia kuwafukuza kazi watumishi hao watatu na kushushwa cheo na mshahara mtumishi mmoja.

Akiwasilisha taarifa ya kuhitimisha mashauri ya nidhamu ya watumishi wanne kwa Baraza maalum la Mashauri ya Nidhamu, Mkuu wa Divisheni ya Utawala na Menejimenti ya Rasilimali watu kwa niaba ya Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma, Gerald Ruzika alisema kuwa mkurugenzi aliunda kamati ya uchunguzi kwa mujibu wa Kanuni ya 45 na 46 ya Kanuni za Utumishi wa Umma za Mwaka 2022 kuchunguza tuhuma dhidi ya watumishi wanne.

Akiongelea mashtaka waliyotuhumiwa nayo alisema kuwa Mteknolojia Maabara alishtakiwa kwa kushindwa kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi kwa sababu ya matumizi ya pombe yaliyokithiri, kutumia bila idhini ya mamlaka vifaa vya umma kwa shughuli zisizohusiana na majukumu yake, kufanya mambo ambayo yanashusha hadhi ya Utumishi wa Umma, kwenda kinyume na maadili ya Utumishi wa Umma na kutokuwepo kazini kwa zaidi ya siku tano bila kuwa na likizo ama ruhusa ya mwajiri.

Kwa upande wa Afisa Muuguzi Msaidizi alishtakiwa kwa kutokuwepo kazini kwa zaidi ya siku tano bila kuwa likizo au ruhusa ya mwajiri.

Muuguzi alishtakiwa kwa kutokuwepo kazini kwa zaidi ya siku tano bila kuwa likizo, ruhusa ya mwajiri au sababu za msingi na kutofanya majukumu aliyopangiwa kama mtumishi wa umma.

Mtendaji wa Mtaa alishtakiwa kwa kutokuwepo kazini bila kuwa likizo, ruhusa au sababu za msingi na kutotekeleza majukumu aliyopangiwa kama mtumishi wa umma.







MKURUGENZI Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, Bi. Erica Yegela, ametembelea banda la Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya (MZRH) katika Maonesho ya Nne ya Biashara na Kilimo (Mbeya City Expo 2026) yanayofanyika kwenye viwanja vya lililokuwa Soko la Zamani la Uhindini Jijini Mbeya.

Akiwa bandani hapo, Bi. Yegela amejionea namna wataalamu wa afya wanavyotoa huduma mbalimbali za kibingwa na kibobezi bila malipo kwa wananchi wanaofika kujitokeza kwenye maonesho hayo makubwa Nyanda za Juu Kusini.

Bi. Yegela ameupongeza Uongozi wa hospitali hiyo chini ya Mkurugenzi Mtendaji, Dkt. Godlove Mbwanji, kwa kusogeza huduma za kisasa na vipimo vya kibingwa karibu na jamii, hatua inayookoa muda na gharama kwa wananchi wa mkoa wa Mbeya na mikoa jirani.

"Nimefarijika sana kuona namna hospitali yetu ya kanda ilivyojipanga vizuri kusogeza huduma hizi kubwa na muhimu hapa kiwanjani. Wananchi wasisubiri hadi wawe wagonjwa sana, waje sasa hivi kupata ushauri na vipimo kutoka kwa madaktari bingwa," alisema Bi. Yegela.

Aidha, ametoa wito kwa wakazi wote wa Mbeya na maeneo ya jirani kujitokeza kwa wingi katika maonesho hayo kuanzia sasa hadi yatakapotamatika tarehe 30 Mei 2026, ili kupata huduma bora za afya pamoja na kujifunza fursa mbalimbali za biashara na kilimo zilizopo mkoani hapo.

Amesema kuwa uwepo wa huduma hizo bure ni fursa ya kipekee ambayo haipaswi kuachwa hivi hivi na wananchi wanaojali afya zao.

Maonesho hayo ya Mbeya City Expo yameandaliwa na Chemba ya Biashara, Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA) kwa ushirikiano na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, yakiwa na lengo la kukuza uchumi, biashara, kilimo, na uwekezaji mkoani humo.

Hadi sasa, maonesho hayo yamevutia taasisi nyingi za kiserikali na binafsi zinazotoa elimu na huduma mbalimbali kwa umma.






📍Mtwara

Mkoa wa Mtwara umeendelea kujidhihirisha kama kitovu muhimu cha uwekezaji wa madini nchini kutokana na uwepo wa rasilimali nyingi za madini ya viwandani, vito na madini mkakati, huku mapato ya Serikali kupitia sekta hiyo yakiongezeka kwa kasi katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita.

Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Mtwara, Winnifrida Mrema, amesema mkoa huo unafahamika zaidi kwa uwepo wa madini ya chokaa yanayotumika kuzalisha saruji katika Kiwanda cha Saruji cha Dangote, jambo linalochangia kukuza uchumi wa mkoa na kuimarisha shughuli za viwanda nchini.

Amesema Mkoa wa Mtwara pia una utajiri wa madini mengine ya viwandani yakiwemo chuma, shaba, kinywe, ulanga pamoja na madini ya mchanga mzito (heavy mineral sands), ambayo ni miongoni mwa madini mkakati yanayohitajika kwa kiwango kikubwa duniani katika utengenezaji wa teknolojia mbalimbali ikiwemo magari ya umeme.

Aidha, amesema Bandari ya Mtwara imeendelea kuwa kiungo muhimu cha biashara na usafirishaji wa madini na bidhaa za viwandani, ambapo hutumika kusafirisha saruji ya Dangote kwenda Zanzibar na Visiwa vya Comoro, sambamba na usafirishaji wa makaa ya mawe kutoka mikoa ya Ruvuma na Njombe kuelekea masoko ya China, India na Dubai.

Kwa upande wa uwekezaji, Mrema amesema Mkoa wa Mtwara una fursa kubwa katika uchimbaji na uchakataji wa madini ya dhahabu, shaba pamoja na vito, hususan green garnet, huku akiwahimiza wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kutumia fursa hizo kuwekeza katika sekta ya madini.

Pia amesema Serikali inaendelea kuwahamasisha wawekezaji kushirikiana na wachimbaji wadogo wa madini ya viwandani, dhahabu na vito kwa kuwapatia mitaji, mafunzo na msaada wa kitaalam ili kuongeza uzalishaji na kuboresha shughuli zao za uchimbaji.

Akizungumzia mapato ya Serikali, Mrema amesema makusanyo kupitia sekta ya madini mkoani humo yameongezeka kutoka shilingi bilioni 1.85 mwaka 2021/22 hadi shilingi bilioni 5.95 mwaka 2023/24, kabla ya kufikia shilingi bilioni 7.55 mwaka 2024/25, hatua inayoonesha ukuaji mkubwa wa sekta hiyo na mchango wake katika uchumi wa taifa.

Naye Fundi Sanifu Madini kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Mtwara, Nurah Juma, amesema madini ya ujenzi kama mawe na kokoto yanayochimbwa katika kijiji cha Chipite wilayani Masasi yameendelea kuwa mhimili muhimu wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika mikoa ya Mtwara na Lindi.

Amesema kokoto zinazozalishwa katika eneo hilo zinatumika katika ujenzi wa barabara, majengo, upanuzi wa Bandari ya Mtwara na viwanja vya ndege, pamoja na ujenzi wa Bandari mpya ya Kisiwa Mgao, hali inayochangia upatikanaji wa vifaa vya ujenzi vyenye ubora na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika ukanda wa kusini.








Na Karama Kenyunko - Michuzi Tv

Wafanyabiashara watatu wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kivukoni wakikabiliwa na tuhuma za makosa ya Uhujumu Uchumi, wakidaiwa kutoa taarifa za uongo kwa maofisa wa forodha wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na kusababisha mamlaka hiyo hasara ya zaidi ya Sh milioni 120.

Washtakiwa hao wanadaiwa kutekeleza makosa hayo katika mipaka ya Sirari mkoani Mara, Mkenda na Kawale mkoani Ruvuma, kwa lengo la kujipatia vibali vya muda vya matumizi ya magari yaliyokuwa yamesajiliwa kwa namba za Afrika Kusini.

Katika hati ya mashtaka iliyosomwa mahakamani na Wakili wa Serikali, Godfrey Nugu akisaidiana na Rozalia Rutagwerela, washtakiwa hao wametajwa kuwa ni George Kaiza (35), Hosiana Sanga (31) na Hamu Sanga (26).

Mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Ramadhani Rugemarila, upande wa mashtaka ulidai kuwa katika kesi namba 11588/2026 inayomkabili George Kaiza pekee, mshtakiwa huyo anakabiliwa na mashtaka saba.

Inadaiwa kuwa Machi 27, 2026 katika mpaka wa Mkenda na Kawale mkoani Ruvuma, Kaiza alitoa taarifa za uongo kwa maofisa wa forodha wa TRA ili kuingiza nchini gari aina ya Toyota Fortuner lenye namba za usajili za Afrika Kusini kwa lengo la kupata kibali cha muda.

Aidha, Februari 25, 2026 katika mpaka wa Sirari mkoani Mara, Kaiza anadaiwa kutoa taarifa za uongo kwa maofisa wa TRA wakati akiingiza nchini gari aina ya Ford Ranger lenye namba za usajili za Afrika Kusini kwa lengo la kujipatia kibali cha muda kwa njia ya udanganyifu.

Upande wa mashtaka ulidai pia kuwa Kaiza aliuza magari hayo kinyume cha sheria huku akijua kuwa yalikuwa yamepewa vibali vya muda na TRA.

Wakili Nugu alidai kuwa Machi 27, 2026 katika mpaka wa Mkenda na Kawale mkoani Ruvuma, Kaiza alikwepa kwa makusudi kulipa ushuru wa zaidi ya Sh milioni 84 kwa magari mawili ambayo ni Toyota Fortuner na Ford Ranger yaliyokuwa na namba za usajili za Afrika Kusini, jambo ambalo alifahamu kuwa ni kinyume na sheria.

Hata hivyo, Kaiza hakutakiwa kujibu chochote mahakamani kwa kuwa Mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi za Uhujumu Uchumi. Upande wa mashtaka ulidai kuwa upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika.

Kwa upande wa washtakiwa Hosiana na Hamu, wanadaiwa kuwa Januari 25, 2026 katika eneo la Tunduma mkoani Songwe walitoa taarifa za uongo ili kujipatia kibali cha muda na kuingiza nchini gari aina ya Ford Ranger lenye namba za usajili za Afrika Kusini.

Inadaiwa kuwa kwa kufanya hivyo, waliisababishia TRA hasara ya Sh milioni 35.5 kutokana na kukwepa kulipa ushuru wa uingizaji wa gari hilo huku wakijua kuwa kitendo hicho ni kinyume cha sheria.

Licha ya dhamana kuwa wazi, hadi wakati Michuzi Blog inaondoka mahakamani, washtakiwa wote walikuwa bado wamerudishwa rumande baada ya kushindwa kutimiza masharti ya dhamana yaliyotaka kila mmoja kuwa na wadhamini wawili, kuweka fedha taslimu sawa na nusu ya kiasi cha hasara kinachodaiwa kusababishwa au kuwasilisha hati ya mali isiyohamishika.

Kesi hiyo imeahirishwa hadi Juni 9, 2026 kwa ajili ya kutajwa.




Na Mwandishi Wetu
URUGENZI Mtendaji wa Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Binafsi (PPP Centre), David Kafulila, amesema mfumo wa Ubia kati ya Serikali na Sekta Binafsi (PPP) ni suluhisho muhimu la kuongeza ufanisi wa viwanja vya ndege, akitolea mfano mafanikio yaliyopatikana katika huduma za Hijja nchini Saudi Arabia.

Kafulila amesema maboresho yaliyofanyika katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa King Abdulaziz (KAIA) uliopo Jeddah yameonyesha namna uwekezaji kupitia PPP unavyoweza kubadili utoaji wa huduma kwa kiwango kikubwa, hasa kwa mahujaji wanaosafiri kuelekea Makka.

Akitoa salamu za Eid al-Adha kwa Waislamu duniani, Kafulila amesema kabla ya maboresho hayo, mahujaji walikuwa wakitumia kati ya saa sita hadi 10 kukamilisha taratibu mbalimbali za uwanjani, hali iliyokuwa ikisababisha usumbufu mkubwa na ucheleweshaji wa huduma.

Hata hivyo, amesema baada ya utekelezaji wa mradi wa PPP wenye thamani ya dola milioni 249 za Marekani, muda huo umepungua kwa kiasi kikubwa hadi kati ya dakika 45 na saa moja, jambo lililoongeza kasi ya huduma na kurahisisha safari za mahujaji.

“PPP imeongeza ufanisi mkubwa sana. Kabla ya mradi huu, uwanja ulikuwa ukihudumia wastani wa mahujaji milioni moja kwa mwaka, lakini sasa unahudumia kati ya abiria milioni nane hadi tisa kwa mwaka,” amesema Kafulila.

Ameeleza kuwa mafanikio hayo yalitokana na utekelezaji wa mkataba wa miaka 20 kati ya Mamlaka ya Anga ya Saudi Arabia (GACA) na kampuni binafsi ya Hajj and Umrah Terminals Development Company, ukihusisha Saudi Binladin Group pamoja na Aéroports de Paris Management huku Shirika la IFC likiwa mshauri mwelekezi.

Kwa mujibu wa Kafulila, uzoefu huo unapaswa kuwa somo kwa Tanzania katika kuimarisha sekta ya usafiri wa anga kupitia mfumo wa PPP ili kuongeza ufanisi wa viwanja vya ndege, kuboresha huduma kwa wasafiri na kuchochea ukuaji wa uchumi.

“Tusiogope kuwakaribisha wawekezaji kupitia PPP kwenye viwanja vyetu vya ndege ili kuongeza ufanisi wa huduma na kuchochea mageuzi ya kiuchumi,” amesema.

Aidha, amesema tathmini ya sekta ya usafiri wa anga duniani ya mwaka 2023 inaonyesha kuwa licha ya viwanja vya ndege vinavyoendeshwa kwa mfumo wa PPP kuwa asilimia 14 pekee duniani, vinahudumia karibu asilimia 40 ya abiria wote duniani.

“PPP na ufanisi ni pacha,” amesema Kafulila huku akiwatakia Waislamu wote Eid Mubarak yenye amani na baraka tele.
-Ni katika mdahalo maalum kwenye Mkutano wa Mwaka wa AfDB

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba ameshiriki mdahalo maalum wa uzinduzi wa taarifa ya African Economic Outlook 2026 ambapo ametoa taswira ya jinsi Tanzania ilivyofanikiwa kuimarisha usimamizi wa fedha za umma na mageuzi katika sekta ya fedha.

Akizungumza katika mdahalo huo jana jioni (Jumanne, Mei 26, 2026) katika ukumbi wa kimataifa wa mikutano wa Kintele (Kintele International Conference Centre), jijini Brazzaville, Jamhuri ya Kongo, Waziri Mkuu alisema Tanzania imeendelea kuchukua hatua za kuimarisha sekta binafsi na kuongeza vyanzo vya mapato ya ndani katika kuimarisha uhamasishaji wa rasilimali za ndani.

“Hatua hizo zinaenda sambamba na uamuzi wa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan wa kuunda tume ya kupitia mifumo ya kodi, usimamizi wa kodi, pamoja na viwango vya kodi, kwa lengo la kufanya mfumo wa ukusanyaji kuwa rafiki zaidi na kuongeza wigo wa mapato ya Serikali.”

Waziri Mkuu alikuwa akijibu swali la mwezeshaji wa mdahalo huo, Dkt. Joy Kategekwa ambaye pia ni Mkurugenzi wa Uratibu na Ushirikiano wa Kikanda wa Benki ya AfDB ambaye alimtaka Waziri Mkuu aeleze uzoefu wa Tanzania katika usimamizi wa fedha za umma na jinsi ambavyo imefanikiwa kufikia bajeti ya nchi inatumia asimilia 70 ya mapato ya ndani.

Akitoa ufafanuzi zaidi, Dkt. Mwigulu alisema Tanzania iliamua kuimarisha ukusanyaji wa mapato kwa kuiongezea ufanisi Mamlaka ya Mapato ikiwemo kuweka mifumo ya ukusanyaji kwa kutumia njia za kidijitali kama vile mashine za EFD na kufanya malipo kwa njia za mitandao ya simu.

“Mamlaka za Serikali za Mitaa ziliimarishwa kwa kuruhusiwa kukusanya mapato yasiyo ya kikodi na tukahakikisha kuwa kunakuwa na nidhamu ya matumizi ya fedha kwa kila senti inayokusanywa (prudency) na wananchi waliona fedha zao zinatumika katika miradi hiyo,” alisema na kuongeza:

“Tanzania ni miongoni mwa wanufaika wa ushirikiano na Benki ya Maendeleo ya Afrika na tumepata nafasi ya kushirikisha uzoefu wetu kuhusu utekelezaji wa miradi mbalimbali kwa kutumia vyanzo vya ndani vya fedha ikiwemo ujenzi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere, miradi ya huduma za jamii, ujenzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma, Hospitali ya Benjamin Mkapa pamoja na miradi mingine ya miundombinu iliyotekelezwa kwa kutumia rasilimali za ndani ya nchi.”

Akitoa maelezo ya jumla kuhusu mkutano huo, Waziri Mkuu alisema wakati wa ufunguzi walijadili ajenda kadhaa ikiwemo ripoti za kifedha na mada zilizohusu uhuru wa kiuchumi wa nchi za Afrika na nafasi ya mawakala wa biashara katika maendeleo ya bara la Afrika.

“Katika ufunguzi, tumeelekeza nguvu kubwa katika kujadili namna ambavyo nchi za Afrika zinaweza kuondokana na utegemezi wa vyanzo vya fedha kutoka nje kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo na badala yake kujikita zaidi katika matumizi ya vyanzo vya ndani vya mapato na rasilimali zilizopo barani Afrika.”

Alisema sababu kubwa ya mjadala huo ni mabadiliko yanayoendelea duniani ambayo yamesababisha baadhi ya vyanzo vya fedha vilivyozoeleka kama vile misaada na mikopo yenye masharti nafuu kuendelea kupungua kutokana na changamoto mbalimbali za kiuchumi zinazozikabili nchi zilizokuwa zikitoa misaada hiyo.

Waziri Mkuu alisema katika mjadala huo imebainishwa wazi kuwa Afrika bado ina fursa kubwa ya kufanikisha miradi yake ya maendeleo kwa kutumia vyanzo vya ndani. “Miongoni mwa maeneo yaliyotajwa ni matumizi ya mifuko ya hifadhi ya jamii, sekta ya bima, rasilimali za asili, pamoja na utajiri uliopo katika nchi mbalimbali za Afrika. Kwa hiyo, mjadala umeonesha kuwa huu ni wakati sahihi kwa Afrika kuelekeza nguvu zake katika kujitegemea kifedha kupitia matumizi bora ya rasilimali za ndani.”

Hata hivyo, Waziri Mkuu ameeleza, ili kufanikisha hilo ni lazima kuwepo na matumizi bora ya rasilimali hizo, pamoja na kuwekeza katika miradi yenye tija kwa wananchi. Miradi hiyo ni ile inayolenga kuzalisha ajira kwa vijana na wanawake, kukuza uchumi, kuongeza mapato ya ndani na kuhakikisha kunakuwa na uendelevu wa mapato ya Serikali.

Ametaja eneo jingine ambalo limeguswa kuwa ni umuhimu wa teknolojia katika kuchochea maendeleo ya kiuchumi kwani itasaidia kuongeza tija katika uzalishaji, kuboresha ukusanyaji wa mapato na kuongeza ufanisi katika usimamizi wa mifumo mbalimbali ya kiuchumi.

Alisema azimio muhimu ambalo nchi washiriki zimeondoka nalo ni umuhimu wa Serikali za Afrika kuwekeza katika mabadiliko ya kisera, kisheria na kiutawala yatakayowezesha matumizi bora ya fursa zilizopo ikiwemo maboresho ya mifumo ya kodi, usimamizi wa mapato yasiyo ya kodi, usimamizi wa miradi ya maendeleo na kuimarisha mifumo ya utawala wa kifedha.






Na Mwandishi Wetu

WAKATI vitendo vya uharibifu wa miundombinu katika miradi mbalimbali ya kimkakati ikiripotiwa kuendelea hapa nchini, Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania, (TPDC) limeimarisha ushirikiano na jamii kwa kutoa elimu kuhusu umuhimu wa kulinda na kuhakikisha usalama wa miundombinu ya bomba la gesi asilia unakuwepo.

Katika Programu ya elimu kwa umma inayolenga kuongeza uelewa wa wananchi wanaoishi karibu na maeneo yanayopitiwa na bomba la gesi asilia iliyofanyika hivi karibuni kwenye vijiji vya Mkwalia Kitumbo na Sunguvuni, wilayani Mkuranga mkoani Pwani, maofisa wa shirika hilo wamesema lengo la elimu hiyo ni kuwafanya wananchi wawe sehemu ya mfumo wa ulinzi wa miundombinu hiyo muhimu kwa maendeleo ya taifa.

Akizungumza wakati wa utoaji wa elimu hiyo, Ofisa Mwandamizi wa Maendeleo ya Jamii wa TPDC, Bw. Oscar Mwakasege alisema mpango huo ni sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa shirika wa kushirikisha wananchi katika kulinda rasilimali za taifa pamoja na kuhakikisha jamii inakuwa na uelewa sahihi kuhusu matumizi salama ya maeneo yanayozunguka bomba la gesi.

Alisema TPDC imeona umuhimu wa kuwafikia wananchi moja kwa moja katika vijiji vyao ili kuwajengea uwezo wa kutambua viashiria vinavyoweza kuhatarisha usalama wa bomba la gesi na namna ya kuchukua hatua mapema.

“Lengo letu ni kuhakikisha wananchi wanaelewa umuhimu wa bomba la gesi asilia, namna ya kulilinda na kutoa taarifa mapema wanapoona viashiria vya uharibifu au shughuli zisizo salama karibu na miundombinu hiyo. Tunataka wananchi wawe walinzi wa kwanza wa rasilimali hii muhimu ya taifa,” alisema Bw. Mwakasege.

Aliongeza kuwa baadhi ya shughuli zinazoweza kuhatarisha usalama wa bomba la gesi ni pamoja na uchimbaji holela karibu na njia ya bomba, ujenzi usioruhusiwa, uchomaji moto ovyo pamoja na vitendo vya uharibifu wa alama za tahadhari zilizowekwa na mamlaka husika.

Kwa mujibu wa Bw. Mwakasege, usalama wa miundombinu ya gesi asilia una mchango mkubwa katika kuhakikisha huduma mbalimbali muhimu zinaendelea kutolewa nchini, ikiwemo uzalishaji wa umeme kwa kutumia gesi asilia, shughuli za viwandani na maendeleo ya sekta nyingine za uchumi.

Aidha alisema ushirikiano kati ya TPDC na wananchi umeendelea kuleta mafanikio katika maeneo mengi yanayopitiwa na bomba hilo, kwani wananchi wengi wamekuwa wakitoa taarifa mapema kuhusu shughuli zinazoweza kuhatarisha usalama wa miundombinu hiyo.

Katika mikutano hiyo ya elimu, wananchi walipata nafasi ya kuuliza maswali mbalimbali kuhusu usalama wa bomba la gesi, matumizi ya ardhi karibu na miundombinu hiyo pamoja na hatua zinazopaswa kuchukuliwa endapo kutatokea hali yoyote ya hatari.

Wananchi walioshiriki katika mikutano hiyo wameipongeza TPDC kwa kuwafikia moja kwa moja vijijini na kutoa elimu inayosaidia kulinda rasilimali za taifa huku ikijenga uelewa wa pamoja kuhusu masuala ya usalama.

Baadhi yao walisema hapo awali kulikuwa na uelewa mdogo kuhusu umuhimu wa bomba la gesi asilia na madhara yanayoweza kujitokeza endapo miundombinu hiyo itaharibiwa, lakini elimu inayotolewa sasa imewasaidia kuelewa wajibu wao kama sehemu ya jamii inayozunguka mradi huo.

Mwananchi mmoja kutoka kijiji cha Sunguvuni alisema elimu hiyo imewapa mwanga mpya kuhusu umuhimu wa kushirikiana na mamlaka katika kulinda rasilimali za taifa.

“Sasa tunajua kuwa bomba hili lina umuhimu mkubwa kwa taifa na hata kwa maendeleo ya wananchi wenyewe. Tuko tayari kushirikiana na TPDC kuhakikisha miundombinu hii inalindwa wakati wote,” alisema.

Kwa upande wake, uongozi wa vijiji vya Mkwalia Kitumbo na Sunguvuni umeeleza kuwa utaendelea kushirikiana na TPDC katika kutoa elimu kwa wananchi na kuhamasisha jamii kuwa sehemu ya ulinzi wa bomba la gesi.

Utoaji wa elimu kwa umma uaendelea kutekelezwa katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Pwani ikiwa ni sehemu ya juhudi za TPDC za kuimarisha usalama wa miundombinu ya gesi asilia na kujenga mahusiano mazuri kati ya shirika hilo na jamii inayozunguka mradi wa gesi asilia.

TPDC imesisitiza kuwa ushirikiano wa wananchi ni nguzo muhimu katika kuhakikisha miundombinu ya gesi asilia inalindwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho pamoja na kuendelea kuchochea maendeleo ya uchumi wa taifa.
Ofisa Mwandamizi wa Maendeleo ya jamii kutoka Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC)Oscar Mwakasege akizungumza na wananchi wa vijiji vya wilaya ya Mkuranga hivi karibuni kuhusu umuhimu wa kulinda miundombinu ya Taifa.

-Kozi mpya kwa wakufunzi zaanza kutolewa rasmi,Mkurugenzi wa Chuo atoa neno 

Na Mwandishi Wetu,Michuzi TV

CHUO Cha  udereva Cha Future World kilichopo eneo la Chanika wilayani Ilala jijini Dar es Salaam kimeendelea kuwanoa madereva wa magari ya abiria na mizigo lengo likiwa kuwajengea uelewa wa elimu ya usalama barabarani ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kutokomeza ajali za barabarani nchini.

Madereva wanaofika katika chuo hicho ni kwa ajili ya  kupata mafunzo zaidi ya udereva sambamba na kupatiwa elimu ya usalama barabarani ambapo wamekuwa wakitoka katika mikoa mbalimbali nchini.

Akizungumza  Mei 26,2026 wakati wa kupokea madereva waliojiunga na chuo hicho,madereva waliomaliza masomo yao kwa kufanya mihatihani pamoja na kutambulisha kozi mpya ya  mafunzo maalum kwa wakufunzi wa udereva ,Mkurugenzi Mtendaji na Mmiliki wa chuo hicho Robert Mkolla ametumia nafasi kueleza kwa kina sababu za ajali za barabarani hatua ambazo chuo kinazichukua kukomesha ajali hizo.

Amefafanua kuna sababu tatu ambazo ndizo zimekuwa chanzo cha ajali  za barabarani na ili kuondoa sababu hizo  ni lazima  dereva kupatiwa elimu na ndio maana chuo hicho kimekuwa mstari wa mbele kutoa elimu kwa madereva nchini.

“Tafiti zinaonesha ajali nyingi za barabarani zinatokana na makosa ya kibinadamu na hasa makosa ya dereva na sababu zinazosababisha ajali hizo ni uzembe, upuuzaji na kutokujua.

“Hakuna binadamu mwenye akili timamu asiyejua madhara ya ajali ,kinachosababisha ajali  ni kutojua ,kupuuza au kuzembea,”amesema na kufafanua sababu hizo zote zinaondolewa kwa dereva kupatiwa mafunzo na elimu ya usalama barabarani.

Kuhusu chuo hicho amesema kimeendelea kuwa Chuo kinachopika madereva ambao wanaweza kuendesha magari ndani na nje ya Tanzania kwani mbali ya kupata mafunzo ya udereva na elimu ya usalama barabarani chuo kina moundombinu yote muhimu sambamba na uwepo wa magari ya kutosha kufundishia huku pia teknolojia katika ufundishaji ikipewa kipaumbele.

Kwa upande wa madereva ambao wanapatiwa mafunzo katika chuo hicho akiwemo Erasto John na George Steven wamesema wamefika kupata mafunzo hayo kwa sababu katika zama hizi hakuna tena ujanja ujanja na Serikali imesimama imara katika kusimamia sheria za usalama barabarani sambamba na kuwa na madereva waliopata mafunzo ya udereva katika vyuo vinavyotambulika.

Wamesema kutokana  na hali hiyo ndio wamelazimika kufika katika chuo hicho ili kupata elimu ya usalama ya barabarani na hasa katika udereva wa kujihami ambapo udereva huo ndio unaepusha ajali za barabarani.

Wameeleza kabla ya kwenda kusoma walikuwa wanaendesha gari bila kuwa na uelewa wa kutosha hasa kutafsiri alama za barabarani lakini kwa sasa wamefahamu na wanauelewa mkubwa kuhusu udereva na sheria zake.

Wakati huo huo wakufunzi Egnas Bethod na Elbariki Juma ambao wametoka vyuo tofauti vya dereva na wapo katika Chuo cha Future World kwa ajili ya kuongezewa ujuzi kupitia kozi ya ukufunzi  wamesema kuna mabadiliko mengi yamekuwa yakitokea katika taaluma ya udereva .

Wamefafanua kutoka mwaka jana hadi sasa mfumo umekuwa wa utoaji leseni umekuwa ukibadilika hasa kwa mamlaka kuweka vigezo vya utoaji leseni.

“Zamani mtu alikuwa anaenda chuo hata kwa siku moja au mbili na anapewa leseni ya udereva.Wapo pia waliokuwa wanapata leseni kwa kuletewa na ndugu zao lakini kwa sasa hakuna njia za mkato,kwa siku hizi lazima ufuate utaratibu uliowekwa na Serikali, hivyo lazima sisi tunaofundisha madereva tuendelee kupata maarifa mapya kwa ajili ya kutuwezesha kuwafundisha madereva.”

Wameongeza kwa siku hizi ili chuo cha udereva kiwe na hadhi ya kutoa cheti kwa wanafunzi lazima wakufunzi na wenyewe wawe na vigenzo ambavyo usajili wake umetoka Jeshi la Polisi , hivyo imewalazimu nao kurudi darasani ili vyuo vyao viwe na sifa ya kutoa vyeti na wanafunzi ambao ni madereva kupata leseni.





Na Mwandishi wetu, Simanjiro 


WANAFUNZI wanamichezo 60 wa shule za msingi wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro wamechaguliwa kuiwakilisha Wilaya hiyo kwenye Umoja wa Michezo na Taaluma Shule za Msingi Tanzania (UMITASHUMTA) katika ngazi ya Mkoa wa Manyara.

Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro, Gracian Max Makota akizungumza wakati akizindua rasmi michuano hiyo katika viwanja vya Mnyalu Complex Mji mdogo wa Mirerani amewaasa wanamichezo hao wanawawakilishe vyema na kuwa washindi katika ngazi ya Mkoa.

"Mrudi na vikombe vya ushindi, mkashindane kwa akili, nguvu maarifa na nidhamu, kwani mchezaji mzuri ni yule ambaye anawasikiliza walimu na kutekeleza yale anavyoelezwa ili kufanikisha ushindi," amesema DED Makota.

Afisa Elimu Msingi na Awali wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro Darous Daudi Limandola amesema wanamichezo 60 wataiwakilisha Halmashauri hiyo kwenye ngazi ya Mkoa wa Manyara.

Limandola amesema wanamichezo hao ni timu iliyosheheni hivyo wanatarajia watarudi na ushindi katika michezo mbalimbali watakavyopambana na wanafunzi wengine wa halmashauri nyingine za mkoa huo.

"Hii ni timu ya ushindi Simanjiro ambayo tunatarajia baadhi ya wachezaji watateuliwa na kushiriki katika timu ya Mkoa wa Manyara kwenda kwenye mashindano ya UMITASHUMTA ngazi ya Taifa," amesema Limandola.

Mratibu wa kambi ya michezo ya UMITASHUMTA ngazi ya Wilaya ya Simanjiro, mwalimu Mshana ametaja michezo itakayopambaniwa na wanafunzi 60 watakaoiwakilisha Simanjiro ngazi ya Mkoa wa Manyara ni soka la wavulana na wasichana, mpira wa pete, mpira wa wavu, riadha, miruko na mitupo, kurusha kisahani na fani za ndani.

Mwalimu Mshana amesema wamekaa kambini kwa siku 10 na wanafunzi hao wanamichezo wakiendelea kufanya mazoezi na kufundishwa na makocha wao.




Na Mwandishi wetu, Simanjiro


HALMSHAURI ya Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara, baada ya kupata mradi wa mpango wa kukabiliana na mabadiliko ya Tabianchi (SCALE), wataalamu mbalimbali wamekuwa wakipita maeneo tofauti yatakayonufaika na mpango huo kwa kutoa elimu kwa jamii.

Wananchi wa Kijiji cha Olchoronyori Kata ya Msitu wa Tembo, wamepatiwa elimu endelevu kuhusu mbinu za kuhimili na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi, ikiwa ni mkakati wa kujenga jamii inayostahimili majanga ya kimazingira.

Elimu hiyo imetolewa kupitia Mpango wa Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi (SCALE), kwa kipindi cha miaka mitano. Lengo likiwa ni kuwajengea wananchi uelewa wa namna ya kuzuia na kukabiliana na majanga kama vile ukame wa muda mrefu, mafuriko, milipuko ya magonjwa, pamoja na tishio la njaa.

Akizungumza katika mkutano wa wananchi uliofanyika katika kijiji hicho mwezeshaji wa mafunzo hayo mhandisi Joanes Martine amewataka wananchi kuwa mabalozi wema katika jamii zao kwa kuhakikisha wanasimamia sheria na taratibu za utunzaji wa mazingira.

“Nawasihi mkawe mabalozi katika jamii zenu. Shirikianeni kwa pamoja kufuata kanuni bora za utunzaji wa mazingira ikiwemo upandaji wa miti, kilimo endelevu, na kukomesha kabisa tabia ya ukataji miti ovyo pamoja na uchomaji mkaa,” alisisitiza mhandisi Joanes.

Pia, mwezeshaji huyo amewataka wananchi kuwa mstari wa mbele katika kuchochea maendeleo kwa kuibua miradi na fursa mpya zitakazovutia uwekezaji zaidi kutoka serikalini, hatua itakayosaidia kukuza uchumi wa jamii hiyo na taifa kwa ujumla.

Hata hivyo, mpango huo unafanyika kwa kuratibiwa na timu ya mabadiliko ya tabianchi kutoka ngazi ya Halmashauri (CCAT) kwa kushirikiana na timu ya mabadiliko ya tabianchi ngazi ya kata (WCAT).

Kata sita za Oljoro namba tano, Shambarai, Msitu wa Tembo, Loiborsoit, Ruvu Remit na Kitwai zinatarajiwa kunufaika na mradi huo wa SCALE.

Mradi huo wa SCALE unatekelezwa katika mikoa 21 ya Tanzania bara katika halmshauri 54 na mikoa mitano ya Zanzibar kwenye Halmashauri 11.



LEO hii kule Ujerumani kunaenda kuwaka moto katika dimba la Red Bull Salzburg Arena kwenye mechi ya kibabe ya fainali ya Conference League kati ya Crystal Palace dhidi ya Rayo Vallecano. Je nani kuibuka bingwa?

Hii ni mechi ambayo zinakutana timu mbili ambazo hazikutarajiwa kufika hatua hii, lakini zimeandika historia kwa njia tofauti kabisa. Fainali hii itachezwa Leipzig, Ujerumani, na mshindi ataandika ukurasa mpya katika historia ya soka la Ulaya.

Kwa upande wa Crystal Palace, huu ni msimu wa ndoto. Timu ya Oliver Glasner imeonyesha mabadiliko makubwa ya kiuchezaji. Palace wamekuwa wakicheza soka la nguvu, kasi na mashambulizi ya moja kwa moja.

Palace wameonyesha uimara mkubwa wa kiulinzi, kasi kwenye mashambulizi ya kushtukiza na uwezo wa kucheza kwa intensity kubwa kwa dakika zote 90. Timu yao imekuwa ikicheza soka la nguvu, presha ya juu na transitions za haraka sana. Kila wanapopata nafasi ya kushambulia, wanafanya hivyo kwa kasi kubwa na kuwapa shida mabeki wa timu pinzani.

Piga pesa leo kwenye michezo ya kasino ya mtandaoni kama vile Keno, Aviator, Poker, Roullette, Wild Icy Fruits, Super Heli na mingine kibao. Jiunge leo kwa kutembelea tovuti ya meridianbet.co.tz au piga *149*10# kisha uanze safari yako ya ushindi.

Lakini upande wa Rayo Vallecano kuna hadithi nyingine ya kuvutia zaidi. Hii ni timu inayocheza kwa nidhamu kubwa sana ya tactical. Rayo si timu ya mastaa wakubwa, lakini wamefika hapa kwa sababu ya mfumo wao wa pamoja, presha kali na kujituma kwa kila mchezaji uwanjani. Wamekuwa wakicheza soka la kujilinda kwa umakini huku wakitafuta nafasi sahihi za kushambulia.

Rayo wameonyesha uwezo mkubwa wa kuvunja mipango ya timu kubwa. Wanajua jinsi ya kuifanya mechi iwe ngumu, kupunguza kasi ya mchezo na kuwafanya wapinzani washindwe kucheza soka lao la kawaida. Hii ndiyo sababu wamekuwa moja ya timu ngumu kucheza nazo katika mashindano haya.

Palace wamemaliza msimu wakiwa nafasi ya 15 ligi kuu ya Uingereza, huku kushinda kombe hili kutawafanya waweze kushiriki kombe la Europa msimu ujao. Wakati Rayo Vallecano wao wamemaliza nafasi ya 8 kwenye msimamo wa ligi huku naye ubingwa huu ni muhimu sana kwake. Bashiri mechi hii.

Kwa ujumla, Crystal Palace wanaonekana kuwa na nguvu zaidi kimwili na wana kasi kubwa ya mchezo, lakini Rayo Vallecano wana nidhamu ya tactical inayoweza kubadilisha kabisa mwelekeo wa mechi. Hii si fainali ya mabingwa wakubwa wa majina, bali ni fainali ya timu mbili zilizopambana kwa moyo mkubwa mpaka kufika hatua hii.


KAMA umechoka michezo ile ile ya kawaida, basi Spinning Buddha imekuja kivingine kabisa ndani ya Meridianbet. Huu ni mchezo unaobeba burudani, nafasi za ushindi na msisimko ambao vijana wengi wanaupenda sasa hivi. Kila raundi inaweza kuwa mwanzo wa mabadiliko makubwa.

Spinning Buddha sio mchezo wa kubahatisha tu, ni nafasi ya kila mchezaji kujaribu bahati yake kwa mtindo tofauti. Haijalishi wewe ni mpya kwenye kasino au tayari ni mkali wa michezo hii, hapa kila mtu ana nafasi ya kuibuka mshindi.

Vilevile, meridianbet wana michezo mingi ya kasino mtandaoni na mechi za kimataifa za kubashiri zenye ushindani mkubwa wa odds. Jiunge leo kwa kutembelea tovuti ya MERIDIANBET au piga *149*10# kisha uanze safari yako ya ushindi.

Muonekano wake umejaa mvuto wa kipekee wenye mandhari za Asia, rangi kali zinazovutia macho pamoja na mistari 15 ya ushindi inayofanya kila raundi iwe tamu kucheza. Ukianza kucheza, hutamani kutoka kirahisi.

Kitu kinachoongeza moto zaidi ni mizunguko ya bure. Ukifanikiwa kupata alama sahihi, ushindi wako unaweza kuongezwa mara mbili na ukajikuta unaendelea kupata mizunguko mingine ya bure mfululizo. Hapo ndipo mchezo unaanza kuwa mkali zaidi.

Kama unapenda michezo yenye burudani, ushindi na nafasi za kutengeneza pesa kwa burudani, huu ndio muda wako wa kuingia Meridianbet na kuijaribu Spinning Buddha. Bahati inaweza kuamua kutua upande wako leo.

Taasisi ya NMB Foundation na Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS) zimesaini makubaliano ya utekelezaji wa pamoja wa Mradi wa TIMIZA Malengo, unaolenga kuwawezesha zaidi ya wasichana na wanawake 10,000 katika halmashauri 36 za mikoa 10 kupitia elimu ya fedha, ujasiriamali, stadi za maisha na huduma za kinga dhidi ya maambukizi ya VVU.

Akizungumza jijini Dodoma wakati wa hafla ya utiaji saini, Meneja Mkuu wa NMB Foundation, Nelson Karumuna, alisema afya na uchumi haviwezi kutenganishwa, hivyo mapambano dhidi ya VVU na UKIMWI yanahitaji kuunganishwa na fursa za kiuchumi kwa vijana, hasa wasichana na wanawake. Alisema NMB Foundation itatumia uwezo na mtandao wa NMB, ikiwemo mawakala zaidi ya 73,000 nchini, kusogeza huduma na maarifa karibu na jamii.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa TACAIDS, Dkt. Adam Mrisho, alisema afya bora kwa vijana ni msingi wa uchumi wa Taifa, hivyo uwezeshaji wa wasichana kwa elimu, stadi za maisha na fursa za kiuchumi ni njia muhimu ya kupunguza mazingira hatarishi yanayoweza kuongeza maambukizi mapya ya VVU.

Dkt. Mrisho alisema Tanzania imepiga hatua katika kupunguza maambukizi mapya kutoka asilimia 0.27 hadi 0.17, lakini akasisitiza kuwa mafanikio hayo yanahitaji ushirikiano endelevu kati ya Serikali, sekta binafsi, taasisi za kiraia na jamii. Makubaliano hayo yanatarajiwa kuimarisha utekelezaji wa Mradi wa TIMIZA Malengo kwa kujenga kizazi chenye afya, ujuzi na uwezo wa kuchangia maendeleo ya Taifa.








 

Yas Tanzania leo imetambulisha rasmi Yas Business, kitengo maalum kinachounganisha huduma zote za mawasiliano na teknolojia kwa taasisi na biashara chini ya mfumo mmoja wa kisasa.

Hatua hii, ambayo ni uwekezaji wa kimkakati, inaonesha dhamira ya Yas ya kuwaunga mkono wafanyabiashara, wakiwemo wadogo na wa kati (SMEs), pamoja na taasisi za umma na nyingine zote, kutumia teknolojia za kisasa za mawasiliano ili kuongeza ufanisi, kuimarisha utendaji kazi na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa unaozidi kutegemea mifumo ya kidijitali.

Kupitia Yas Business, taasisi na biashara watanufaika na huduma mbalimbali za mawasiliano ya kisasa na teknolojia zikiwemo mifumo ya kuunganisha matawi ya biashara kwa njia salama na ya haraka ( SD-WAN), huduma za kuhifadhi na kutumia taarifa kupitia mtandao (cloud connectivity), teknolojia ya kuunganisha vifaa na mifumo kupitia mtandao (IoT services), huduma za usimamizi wa mifumo ya mawasiliano (managed solutions) pamoja na kituo cha kisasa cha kuhifadhi na kusimamia taarifa za kidijitali (Tier 3 Data Centre infrastructure).

Huduma hizi ni mahsusi kwa ajili ya kuzisaidia taasisi na biashara kuboresha mawasiliano, kuongeza usalama wa taarifa, kurahisisha utekelezaji wa shughuli za kila siku na kuongeza uwezo wa kukuza biashara kwa ufanisi zaidi.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo Waziri wa Nchi, Mipango na Uwekezaji, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo aliipongeza Yas kwa uwekezaji wake katika miundombinu ya mawasiliano ya kisasa na mifumo ya huduma endelevu za kidijitali, hatua inayochangia kwa kiasi kikubwa azma ya Tanzania ya kujenga uchumi wa viwanda jumuishi.

“Mipango ya uwekezaji kama Yas Business ina mchango mkubwa katika kuongeza uzalishaji, ubunifu na matumizi ya teknolojia katika sekta mbalimbali za uchumi. Ushirikiano kati ya sekta ya umma na sekta binafsi utakuwa msingi muhimu katika kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050,” alisema Waziri Kitila

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa Yas, Pierre Canton-Bacara, alisema utambulisho wa Yas Business ni mwendelezo wa dhamira ya muda mrefu ya kampuni hiyo ya kuwa mshirika wa kuaminika wa teknolojia kwa taasisi na biashara nchini.

“Yas Business inaunganisha uwezo wetu wa kuhudumia taasisi na wafanyabiashara chini ya mfumo mmoja imara na wa kisasa unaolenga kuongeza ufanisi, kupanua wigo wa shughuli za biashara na kufungua fursa mpya kupitia huduma bora za mawasiliano na teknolojia za kisasa,” alisema Pierre.

Aliongeza kuwa Yas itaendelea kuunga mkono juhudi za Serikali na taifa kwa ujumla katika kukuza uchumi wa kidijitali kwa kuwekeza katika miundombinu na teknolojia zinazochochea ubunifu, kuongeza uzalishaji na kuimarisha juhudi za ujenzi wa taifa.

Yas Business inahudumia sekta mbalimbali muhimu zikiwemo fedha, usafirishaji na ugavi, viwanda, elimu pamoja na huduma za serikali.

Uwekezaji huu unaendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 pamoja na Mkakati wa Taifa wa Uchumi wa Kidijitali wa mwaka 2024 hadi 2034 (DESF 2024–2034), kwa kuchangia upanuzi wa miundombinu ya mawasiliano ya kisasa, matumizi ya teknolojia katika taasisi na biashara pamoja na ongezeko la uzalishaji.

Ikiungwa mkono na mtandao mpana na imara zaidi nchini Tanzania pamoja na huduma bora kwa wateja, Yas Business ina nafasi nzuri nan kubwa ya kusaidia taasisi na wafanyabiashara kuendesha shughuli zao kwa njia ya kidijitali kwa usalama zaidi, kuimarisha usalama wa mifumo ya taarifa na kuongeza matumizi ya huduma za teknolojia za kisasa.












 


Top News