Na Mwandishi Wetu — Dar es Salaam, 12 Februari 2026

Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) kimeongoza mdahalo wa kitaalamu uliolenga kujadili matumizi ya Akili mnemba (Artificial Intelligence – AI) katika kuboresha utoaji wa huduma za umma na kuongeza ufanisi wa kiutendaji serikalini. Mdahalo huo umefanyika katika Kituo cha Mafunzo kwa Njia ya Mtandao (Global Learning Section – GLS) cha Chuo hicho, jijini Dar es Salaam, na umefunguliwa rasmi na Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bw. Xavier Mrope Daudi.
Akizungumza wakati wa ufunguzi, Bw. Mrope alisema serikali inaendelea kuhimiza matumizi sahihi ya teknolojia za kisasa kama sehemu ya mikakati ya kuboresha utoaji wa huduma bora kwa wananchi, kupunguza gharama za rasilimali fedha na kuongeza uwazi katika taasisi za serikali. Alilipongeza Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kwa kuandaa mdahalo huo muhimu ambao unatoa jukwaa kwa watumishi wa umma, wataalamu wa teknolojia na wadau wengine kubadilishana uzoefu na maarifa kuhusu matumizi ya Akili mnemba katika kuongeza tija na ufanisi wa kazi.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa matumizi yenye uwiano wa maadili na teknolojia, akibainisha kuwa Akili mnemba inapaswa kusaidia katika utendaji wa kazi bila kuchukua nafasi ya utu wa binadamu.

“Akili mnemba haichukui nafasi ya mtumishi wa umma, bali ni nyenzo ya kumsaidia kutoa huduma bora, zenye ufanisi na huruma kwa wananchi,” alisema Bw. Mrope kwa msisitizo.

Akihitimisha hotuba yake, Bw. Mrope alizitaka taasisi za serikali, hususan zile zinazoshughulika na teknolojia ya habari na mawasiliano, pamoja na Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, kuendelea kufanya tafiti na kuibua ubunifu katika matumizi ya teknolojia serikalini. Alisema maoni na mapendekezo yatayotokana na mdahalo huo yatasaidia serikali kuboresha sera na miongozo ya matumizi ya teknolojia kwa kuzingatia DIRA ya Taifa 2050 na mipango ya maendeleo endelevu.

Awali, Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu wa TPSC, Dkt. Ernest Mabonesho, amesema chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kimejipanga kuhakikisha kinaendelea kuwa nguzo muhimu katika kukuza ubora wa utumishi wa umma kupitia mafunzo, mijadala ya kitaalamu na tafiti za teknolojia. Ameeleza kuwa mjadala wa mwaka huu unalenga kujadili namna Akili Mnemba inavyoweza kuboresha utoaji wa huduma serikalini, kuimarisha maamuzi ya kiutawala na kushughulikia masuala ya maadili bila kuvunja misingi ya mtumishi wa umma.

Mdahalo huo ulimewakutanisha watunga sera, wataalamu wa teknolojia, wanasayansi wa data, wasomi pamoja na wawakilishi kutoka wizara, taasisi, idara na wakala mbalimbali za serikali. Washiriki walijadili ana kwa ana na wengine walishiriki kwa njia ya mtandao, hatua iliyoufanya kuwa mjadala wa kina, shirikishi na wenye tija katika kuimarisha matumizi ya teknolojia ya Akili mnemba ndani ya utumishi wa umma nchini.











 

 

Na Mwandishi Wetu

NAIBU Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Xavier Daudi, amesema Serikali imejipanga kikamilifu kutumia Teknolojia ya Akili Mnemba (Artificial Intelligence – AI) ili kuongeza ufanisi, kasi na ubora wa utoaji huduma kwa wananchi, kufuatia mabadiliko makubwa ya kidunia katika sekta ya teknolojia.

Daudi aliyasema hayo jijini Dar es Salaam leo, Februari 12, 2026, wakati akifungua mdahalo kuhusu matumizi ya Akili Mnemba (AI) katika kuboresha huduma kwa umma, ulioandaliwa na Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC).

Alisema kuwa licha ya Serikali kuendelea kutumia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika miaka ya hivi karibuni, kasi ya ukuaji wa teknolojia ya Akili Mnemba imeleta mazingira mapya yenye changamoto na fursa katika utumishi wa umma, hivyo kuna umuhimu wa kuendana na mabadiliko hayo.

“Ni dhahiri kuwa mabadiliko ni makubwa katika mazingira na kasi ya ukuaji wa teknolojia. Hatuwezi kubaki nyuma wakati dunia inakwenda kwa kasi. Nasi Serikalini tunapaswa kutumia teknolojia ya akili mnemba kuhakikisha wananchi wanafaidika na huduma zinazotolewa kwa haraka na kwa ufanisi zaidi,” alisema Daudi.

Alieleza kuwa matumizi ya teknolojia hiyo yataisaidia Serikali kupata majawabu sahihi kwa wakati, kutatua changamoto za wananchi kwa ufanisi, na kuwafikia kwa wakati muafaka.

Aidha, alisisitiza kuwa Serikali haijakaa kimya katika suala hilo, bali tayari imeanza kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha mifumo ya utoaji huduma kwa kutumia teknolojia za kisasa. Alitolea mfano eneo la ajira, ambapo mifumo ya kidijitali imeanza kutumika kuboresha mchakato huo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), Dkt. Ernest Mabonesho, alisema matumizi ya Akili Mnemba katika utumishi wa umma ni hatua muhimu itakayorahisisha utoaji wa huduma na kuongeza ufanisi kwa watumishi.

“Kazi yetu kubwa ni kutoa mafunzo kwa watumishi wa umma, hasa katika mambo mapya yanayoibuka. Utumishi wa umma unabadilika,” alisema Dkt. Mabonesho.

Alibainisha kuwa ingawa Akili Mnemba ni dhana mpya katika utumishi wa umma, ni teknolojia isiyoweza kuepukika.

“Hii ni teknolojia ambayo inatulazimisha tuanze kuitumia kwa sababu inaleta wepesi katika utoaji wa huduma kwa wananchi, pamoja na kuongeza uwazi na ufanisi,” aliongeza.

Naye mshiriki wa mdahalo huo, Mahyolo Kalokola, alisema mjadala huo umemfungua macho kuhusu fursa zilizopo katika matumizi ya Akili Mnemba.





 

Na Mwandishi Wetu, Ngorongoro.

Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya eneo la Ngorongoro (NCAA) Bw. Abdul-Razaq Badru ameongoza kikao cha kimkakati kilichojumuisha waheshimiwa Madiwani,  Viongozi wa Mila, watendaji wa kata, wenyeviti wa Vijiji na watendaji wa vijiji kwa lengo la kudumisha mahusiano na uboreshaji wa huduma za kijamii na uboreshaji wa shughuli  za Uhifadhi shirikishi.

Kamishna Abdul-Razaq Badru ameeleza kuwa kikao hicho ni sehemu ya mkakati wa Mamlaka hiyo kukutana na makundi mbalimbali kujadili uboreshaji wa shughuli za kijamii na huduma za wananchi kama Maji, shule, Malisho, barabara, mawasiliano, afya na mengineyo.

"Viongozi na Wananchi wa Tarafa ya Ngorongoro ni wadau muhimu katika hifadhi, tunakutana nao kama sehemu ya kuboresha uhusiano na kuwaeleza mikakati ya Serikali dhidi yao. 

 kwa sasa tunaboresha miundombinu ya huduma za maji, ujenzi wa Barabara kwa tabaka gumu kutoka Loduare hadi Golini, kujenga minara mipya ya mawasiliano 9 ndani ya hifadhi ili kufikisha huduma kwa wananchi na wadau mbalimbali" amefafanua Kamishna Badru.

Kwa upande wa Viongozi waheshimiwa Madiwani, viongozi wa Mila wameiomba Serikali kupitia Mamlaka hiyo kuendelea kuboresha mahusiano, huduma za kijamii kama  miundombinu ya Maji, barabara, ukarabati wa vituo vya afya na shule, mahitaji  ya baraza la wafugaji, chunvi za mifugo na mpango wa malisho ya mifugo hawa wakati wa kiangazi.












 

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

MKUTANO Mkuu wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji 2026 umeanza rasmi jijini Dodoma kwa mijadala mizito inayolenga kuimarisha sekta ya utangazaji nchini. Mkutano huo wa siku mbili ulioanza leo Februari 12, 2026 unatarajiwa kuhitimishwa kesho Februari 13, 2026.

Mkutano huo umeandaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) ukishirikisha wadau mbalimbali wa sekta ya habari wakiwemo wamiliki wa televisheni, redio na majukwaa ya mitandao ya kijamii kutoka maeneo mbalimbali ya nchi.

Akiwasilisha mada ya kwanza, Mhandisi Andrew Kisaka kutoka TCRA alizungumzia matokeo na utekelezaji wa mapendekezo yaliyotokana na utafiti wa huduma za utangazaji nchini. Alieleza hatua zilizochukuliwa kuboresha ubora wa maudhui, kuimarisha usimamizi wa leseni pamoja na kuzingatia weledi katika utoaji wa taarifa kwa umma.

Wasilisho la pili lilitolewa na Mhadhiri Msaidizi Zuhura Selemani ambaye alielezea fursa na faida za uwekezaji wa teknolojia katika utangazaji vijijini. Alisisitiza umuhimu wa kutumia teknolojia za kisasa kufikisha taarifa kwa wananchi wa maeneo ya pembezoni na kuongeza ushiriki wao katika maendeleo ya taifa.

Kwa upande wake, Nancy Mwaisaka kutoka UNESCO aliwasilisha mada kuhusu TEHAMA na huduma za utangazaji wa redio vijijini, akitoa uzoefu wa taasisi hiyo katika kusaidia redio za kijamii. Alibainisha kuwa redio za vijijini zina mchango mkubwa katika kuelimisha jamii na kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Washiriki wa mkutano huo wanatarajiwa kujadili kwa kina changamoto na fursa zilizopo katika sekta ya utangazaji, huku wakitoa mapendekezo yatakayosaidia kuboresha mazingira ya kazi na kulinda maslahi ya umma katika upatikanaji wa taarifa sahihi na kwa wakati.




 

SERIKALI imetangaza neema ya kihistoria kwa wanablogu, vijana wabunifu, na watoa maudhui mtandaoni nchini kwa kupunguza ada za leseni kwa kiwango kikubwa, hatua inayolenga kuchochea ukuaji wa uchumi wa kidijitali na kurasimisha shughuli za wahabarishaji wa mitandao.

Hatua hiyo imekuja kufuatia utafiti wa kina na mikutano ya kimkakati ya takribani mwaka mzima kati ya mtandao wa Tanzania Bloggers Network (TBN) na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), ikielezea vikwazo vya gharama vilivyokuwa vikikwaza uandishi wa habari za kidijitali nchini.
Akizungumza katika ufunguzi wa Mkutano wa Mwaka wa Watoa Huduma za Utangazaji (ABC 2026) jijini Dodoma leo, Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamisi Mwinjuma, amesema ada ya leseni kwa watoa maudhui mtandaoni imeshushwa kutoka Sh500,000 hadi Sh50,000 tu, huku ada ya maombi ikiwa ni Sh10,000 pekee.

Mageuzi hayo pia yamegusa kundi la wakusanyaji wa maudhui (Online Content Aggregators), ambao ada yao imeshushwa kutoka Sh1,000,000 hadi Sh100,000 pekee. Aidha, kundi la "Amateteur" limeanzishwa kwa ajili ya vijana wanaochipukia ili waweze kujitambulisha rasmi na kukuza vipaji vyao bila vikwazo vya kifedha.

Mapinduzi ya Teknolojia ya DSB
Wakati neema hiyo ikitangazwa, Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Dkt. Jabiri Bakari, ametangaza kuanza kwa teknolojia mpya ya utangazaji wa redio ya kidijitali nchini inayojulikana kama Digital Sound Broadcasting (DSB).

Teknolojia hiyo itaanza kufanya kazi katika mikoa mitano ya majaribio ya Dar es Salaam, Dodoma, Mwanza, Arusha, na Mbeya, lengo likiwa ni kuongeza ubora wa sauti na huduma za utangazaji nchini.

"Tumekamilisha maandalizi yote ya kiudhibiti na watoa huduma wa miundombinu wameshapatikana. Hii ni hatua kubwa ya kuendana na mabadiliko ya teknolojia duniani na kuimarisha utangazaji, hususan maeneo ya vijijini," alisema Dkt. Bakari.

Utafiti: Redio Bado ni Kinara
Katika mkutano huo, Injinia Andrew Kisaka wa TCRA amewasilisha matokeo ya utafiti wa hali ya utangazaji kwa mwaka 2025/2026, ukionyesha kuwa redio inaendelea kuwa chanzo kikuu cha habari kwa asilimia 85 ya Watanzania. Hata hivyo, utafiti huo umebaini ukuaji mkubwa wa matumizi ya intaneti miongoni mwa vijana, ambapo asilimia 45 hupata habari kupitia mitandao ya kijamii kabla ya kusikiliza redio au kutazama televisheni.

Upande wa televisheni, utafiti unaonyesha asilimia 65 ya watazamaji wanatumia ving'amuzi, huku maudhui ya ndani yakipendwa zaidi kwa asilimia 70. Serikali imewahimiza watoa huduma za kienyeji kuwekeza zaidi kwenye majukwaa ya kidijitali (OTT) ili kukidhi mahitaji ya soko la sasa.

Ulinzi wa Hakimiliki na Mikopo
Ili kuhakikisha wanahabari wa kidijitali wanufaika na kazi zao, Serikali imezielekeza taasisi za COSOTA na TCRA kuandaa mpango wa kulinda hakimiliki na kudhibiti uharamia mtandaoni. Aidha, Serikali imeanza kutoa mikopo ya masharti nafuu kwa watengeneza maudhui kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya kisasa vya kufanyia kazi.

Hadi kufikia Desemba 2025, TCRA imetoa jumla ya leseni 707 za utangazaji, zikiwemo 318 za maudhui mtandaoni, jambo linaloashiria kukua kwa uhuru wa habari na demokrasia nchini chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.










 

Manyoni, Singida, Februari 12, 2026 — Ziara ya mafunzo ya wataalamu wa Idara ya Misitu Zanzibar imeingia siku ya pili leo kwa ujumbe huo kuanza rasmi mafunzo ya vitendo katika Shamba Darasa la Nyuki la TFS, wilayani Manyoni.

Mafunzo hayo yameanza kwa mada ya uanzishaji na usimamizi bora wa Hifadhi za Nyuki (Bee Reserves) iliyowasilishwa na Askari wa Uhifadhi – Ufugaji Nyuki Wilaya ya Manyoni, Jacline Leshabari, akieleza hatua za kisheria, kiutawala na kiikolojia zinazohitajika katika kuanzisha na kulinda maeneo maalum ya nyuki.

Akiwasilisha mada hiyo, Leshabari amesema hifadhi za nyuki zimekuwa nyenzo muhimu si tu katika kuongeza uzalishaji wa asali na mazao yatokanayo na nyuki, bali pia katika kulinda misitu na bioanuai. “Usimamizi madhubuti wa hifadhi hizi unahakikisha upatikanaji endelevu wa malighafi za nyuki huku ukihifadhi mfumo wa ikolojia,” amesema.

Kwa mujibu wa ratiba ya mafunzo, wataalamu hao kutoka Zanzibar wanatarajiwa pia kujionea kwa vitendo utambuzi wa maeneo ya hifadhi, uwekaji wa mizinga ya kisasa, pamoja na mbinu za kushirikisha jamii katika kulinda na kunufaika na rasilimali za nyuki.

Mkurugenzi wa Idara ya Misitu Zanzibar, Said Juma Ali, amesema mafunzo ya siku ya pili yamewapa mwanga mpana juu ya namna TFS inavyounganisha uhifadhi na uchumi wa jamii kupitia sekta ya nyuki. Amesisitiza kuwa uzoefu huo utasaidia Zanzibar katika mpango wake wa kuanzisha hifadhi za nyuki na kuendeleza utalii wa nyuki.

Ziara hiyo ya siku tano inatarajiwa kuendelea kwa mafunzo zaidi kuhusu uchakataji wa asali, viwango vya ubora na masoko, huku ushirikiano kati ya TFS na Idara ya Misitu Zanzibar ukitajwa kuwa kichocheo cha mageuzi ya sekta ya nyuki nchini.




 

Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Elimu Tanzania Dkt. Aneth Komba amesema, Serikali imetoa vitabu vya masomo ya Elimu ya Amali bure kwa shule zote za umma na binafsi ili kuongeza hamasa katika ufundishaji na ujifunzaji wa masomo hayo yatayosaidia kukabiliana na changamoto ya ajira kwa mwanafunzi pindi wanapohitimu.

Dkt. Komba amesema hayo leo Februari 12, 2026 katika zoezi la ugawaji wa vitabu vya Amali kwa wakuu wa shule zote Tanzania Bara ambazo zinatoa Elimu ya Sekondari katika mkondo huo.

Amesema, mwaka 2024 Serikali ilianza kutekeleza Mtaala uliobereshwa ambao umegawanyika katika mkondo wa Amali na mkondo wa jumla, huku akisisitiza mkondo wa Amali lengo lake ni kujenga Elimu ujuzi kwa mwanafunzi.

Sambamba na ugawaji wa vitabu vya Amali, Dkt. Komba amesema, TET imetoa mafunzo kwa wakuu wa shule wote kuhusu maboresho yaliyofanyika kwenye Mtaala hasa katika mkondo wa Amali, pamoja na namna kutumia Maktaba mtandao ambapo vitabu vyote hupatikana.

Aidha, Dkt Komba amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha zilizosaidia upatikanaji wa vitabu nchini, hasa vitabu vya Amali ambavyo vinagawiwa bure kwa shule zote nchini za Serikali na za binafsi.

Nae, Meneja uchapaji na usambazaji wa vitabu Taasisi ya Elimu Tanzania Bw. Emmanuel Stanslaus ametoa wito kwa walimu kuhakikisha wanatua vitabu hivyo kwa usahihi ili vilete tija kwa wanafunzi kulingana na fani wanazosoma.

Kwa upande wake Mkuu wa shule ya ufundi Nzega na Makamu Mwenyekiti wa wakuu wa shuke Tanzania Bara Mwl. Mwanakombo Juma Martin amesema vitabu hivyo vilivyotolewa bure kwa shule za Serikali na binafsi vitasaidia katika ufundishaji na ujifunzaji kwa wanafunzi hivyo kuleta tija katika utekelezaji wa Mtaala ulioboreshwa mkondo wa Amali.

Nae, Mkuu wa shule ya Ufundi ya wavulana Bwiru iliyopo Mkoani Mwanza Mwl. Thomas Werema amesema Elimu ya Amali inaenda kuwa Mkombozi kwa vijana wa Tanzania, kwani hutoa fursa kwa mw anafunzi kujiajiri, kuajiriwa au kuajiri wengine pindi amalizapo masomo yake, hivyo kusaidia kukabiliana na changamoto ya ajira nchini.













Top News