Wafanyakazi wa EWURA wakishiriki maandamano ya Mei Mosi mbele ya Rais, Mhe. Samia Suluhu Hassan.


...


Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) leo, Mei 1, 2026, imeungana na wafanyakazi wengine duniani kuadhimisha Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi), maadhimisho yaliyofanyika kitaifa mkoani Njombe.

Sherehe hizo zilihudhuriwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ambaye alikuwa mgeni rasmi. Katika hotuba yake, Rais Samia amewahimiza waajiri na waajiriwa kote nchini kuendeleza ushirikiano, kuaminiana, na kutanguliza maslahi ya taifa katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kuboresha mazingira na ustawi wa wafanyakazi, huku akiwataka kuongeza bidii na ufanisi kazini. Aidha, alibainisha wazi kuwa Serikali inathamini mchango wa wafanyakazi na itaendelea kuwaunga mkono katika juhudi za maendeleo ya nchi.

Katika maadhimisho hayo, EWURA imewakilishwa na wafanyakazi wake bora kutoka idara na vitengo mbalimbali. Wafanyakazi hao walichaguliwa kwa kura za wenzao kwa kuzingatia vigezo muhimu kama vile utendaji uliotukuka, nidhamu ya kazi, ubunifu pamoja na kujituma kazini.

Wawakilishi hao walishiriki katika maandamano rasmi yaliyopita mbele ya mgeni rasmi, wakibeba mabango yenye ujumbe wa kuhamasisha mshikamano na uwajibikaji kazini.

Ushiriki wao umeonesha dhamira ya EWURA kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi na kuchangia maendeleo ya taifa kwa ujumla.



Wafanyakazi wa EWURA wakishiriki maandamano ya Mei Mosi mbele ya Rais, Mhe. Samia Suluhu Hassan.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwapungia mkono wafanyakazi wa EWURA, wakati wa maandamano ya Maadhimisho ya Sherehe za Meimosi leo.

Na Mwandishi Wetu.

WABUNGE wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  wameshiriki katika semina kuhusu Mpango Mkakati wa Gridi ya Maji ya Taifa.

Semina hiyo imefanyika katika ukumbi wa Bunge wa Msekwa,Dodoma.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji Mhandisi Mwajuma  Waziri katika mada yake amesema Gridi ya  Maji ya Taifa ni mfumo wa kimkakati wa usambazaji maji kutoka kwenye vyanzo vya uhakika na kuyapeleka katika maeneo yenye uhaba wa maji nchini.

Ameongeza hadi sasa  Wizara ya Maji imekamilisha vipande vya  mtandao wa Taifa wa maji ikiwamo kutoa maji ziwa Victoria kwenda mikoa ya Shinyanga, Tabora na Shelui katika mkoa wa Singida.

Kwa upande wake Waziri wa Maji  Jumaa Aweso akihitimisha mada amewaomba ushirikishwaji  wa jamii na  ushirikiano kwa wabunge wote ili kuhakikisha mpango mkakati wa Gridi ya Maji ya Taifa unafanikiwa ili kuhakikisha wananchi wote  wanapata huduma ya majisafi na salama na kuchochea ukuaji wa uchumi ili kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo (DIRA 2050).









Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Albert Chalamila ameongoza mamia ya wafanyakazi Mkoani humo katika maadhimisho ya siku ya wafanyakazi Duniani Mei Mosi yaliyofanyika kimkoa kwenye viwanja vya Mnazi mmoja na kuwataka wafanyakazi kufanya kazi kwa bidii na maarifa huku wakifanya tathmini ya matokeo ya mafanikio au tija ya utendaji wao kwenye taasisi wanazozifanyia kazi

Akizungumza kwenye maadhimisho hayo RC Chalamila amewataka wafanyakazi kutumia nguvu na maarifa yao vizuri kwenye kutekeleza wajibu wao wawapo kazini lakini pia kila mfanyakazi kutafakari mchango wake kwenye taasisi au mamlaka anayoifanyia kazi ili wanapopaza sauti zao kwa ajili ua stahiki zao utendaji wao pia uwe na tija kwenye taasisi zao

Aidha ametumia nafasi hiyo kuwapongeza waajiri wa sekta binafsi kwa kuisaidia Serikali kupunguza changamoto ya ukosefu wa ajira huku akiwataka kifuata taratibu, kanuni na sheria za kazi ili kupunguza malalamiko kutoka kwa wafanyakazi na ameweka msisitizo kwa wafanyakazi kutekeleza wajibu wao kwa ufanisi

Sanjari na hayo Mkuu wa Mkoa Mhe Albert Chalamila amewapongeza wafanyakazi Mkoani humo kwa kazi nzuri wanazozifanya huku akiendelea na msimamo wake wa kuzitaka taasisi kutoa zawadi ya pesa taslimu hadharani kwa watumishi waliofanya vyema kwenye utumishi wao

Akisoma risala ya wafanyakazi Mkoani humo kwa niaba ya katibu mkuu wa chama cha wafanyakazi Mkoa wa Dar es Salaam, Katibu wa Chama cha Walimu Mkoani humo Abraham Kamwela ameishukuru Serikali ya awamu ya sita kwa kuendelea kuboresha mazingira, haki na maslahi kwa wafanyakazi huku akiiomba serikali kuendelea kuboresha mazingira ya kazi ikiwemo kupunguza mfumuko wa bei, kupunguza msongamano wa magari, kuwezesha uwepp wa nyumba za gharama nafuu lwa wafanuakazina kuendelea kuboresha vipato vya wafanyakazi hasa ikizingatiwa changamoto ya ongezeko la gharama za maisha kwa kila nyanja

Maadhimosho hayo ya Mei Mosi yamebeba kaulimbiu isemayo "Kazi zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050"










Ubalozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Zimbabwe umeadhimisha miaka 62 ya Muungano wa Tanzania katika hafla iliyofanyika katika ukumbi wa Hyatt Regency Harare Zimbabwe.

Katika hafla hiyo, Balozi wa Tanzania nchini Zimbabwe, Kamishna wa Polisi (CP) Suzan Kaganda, alipata fursa ya kumkaribisha Fredrick Shava, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia wa Zimbabwe, aliyemwakilisha Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara za Kimataifa, Prof. Amon Murwira, aliye mwakilisha mgeni rasmi.

Akizungumza katika maadhimisho hayo yaliyobeba kauli mbiu isrmayo Miaka 62 Muungano amani umoja na Mshikamano ni Msingi wa Maendeleo endelevu, Balozi Kaganda alishukuru Serikali ya Zimbabwe, jumuiya za kidiplomasia na wadau mbalimbali kwa ushirikiano wao na Tanzania katika kukuza maendeleo huku akisisitiza kuwa Tanzania inaendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ambayo yameleta matokeo chanya.

Kwa upande wake, Waziri Shava aliipongeza Tanzania kwa kudumisha umoja na amani kwa miaka 62 ya Muungano, akieleza kuwa nchi hiyo imekuwa mfano bora katika ukanda wa SADC na Afrika kwa ujumla huku akibainisha kuwa Zimbabwe itaendelea kuthamini mchango wa Tanzania katika harakati za ukombozi na kudumisha ushirikiano wa maendeleo kati ya nchi hizo mbili.









Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Dodoma, Dkt. Neema Peter Majule, ameibua mjadala bungeni kuhusu uwazi na haki katika biashara ya kaboni, akitaka serikali kueleza mikakati iliyopo kuhakikisha wananchi wa chini, hususan wanawake na vijana, wananufaika ipasavyo.

Akizungumza Bungeni Jijini Dodoma, Dkt. Majule alitaka kujua ni viashiria gani na mfumo gani serikali imeweka kuhakikisha makisio ya mapato yanayotokana na misitu na ardhi ya wananchi yanazingatiwa kwa usahihi katika biashara hiyo inayohusisha wawekezaji.

Akijibu hoja hiyo, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Festo Dugange, alikiri kuwepo kwa changamoto za ukosefu wa uwazi katika vipimo na malipo ya biashara ya kaboni kutokana na ushirikiano kati ya wadau mbalimbali.

Dugange alieleza kuwa serikali imeanza hatua za makusudi za kuboresha mfumo huo kupitia uanzishwaji wa kituo maalum cha kuratibu biashara ya kaboni kilichopo Morogoro, ambacho kinatarajiwa kuhamishiwa Dodoma.

Alisema kituo hicho kitashirikiana na wadau na serikali kuhakikisha vipimo sahihi vya kaboni vinapatikana na wananchi wananufaika moja kwa moja kulingana na kiwango halisi cha kaboni kinachozalishwa katika maeneo yao. 



KUNDI la Kimataifa la Vijana wa Amani (IPYG) limeendesha programu jumuishi ya amani na usalama katika eneo la Mwenge, jijini Dar es Salaam, Aprili 2026, chini ya kaulimbiu “Elimisha Amani, Hakikisha Usalama: Ibara ya 10 ya DPCW.” Mpango huo uliunganisha shughuli za uhifadhi wa mazingira na mafunzo ya vitendo ya usalama, ukiwa na lengo la kukuza utamaduni wa amani sambamba na kuimarisha ustahimilivu wa jamii

Azimio la Amani na Kusitishwa kwa Vita (DPCW) ni mfumo wa kimataifa unaobainisha misingi ya kumaliza vita na kuendeleza amani endelevu, ambapo Ibara ya 10 inasisitiza umuhimu wa kueneza utamaduni wa amani.

Kama sehemu ya programu hiyo, zoezi kubwa la plogging lilifanyika katika Makutano ya Mwenge na Kituo Kipya cha Mabasi cha Mwenge. Zaidi ya vijana 300 pamoja na wakazi wa eneo hilo walishiriki kukusanya na kuchambua taka, hatua iliyochangia kuboresha mazingira ya eneo hilo.

Sambamba na usafi huo, kulifanyika kampeni ya uhamasishaji wa umma inayozingatia Ibara ya 10 ya DPCW chini ya kaulimbiu “Elimisha Amani, Hakikisha Usalama.” Kampeni hiyo iliunganisha elimu ya amani na mafunzo ya vitendo ya usalama, ikihamasisha vijana kushiriki kikamilifu katika kulinda jamii zao.

Kwa kushirikiana na Dingonet, shirika lisilo la kiserikali linalojihusisha na usimamizi wa majanga, programu hiyo ilijumuisha maonesho ya matumizi sahihi ya vizima moto na taratibu za kukabiliana na dharura. Washiriki walipata fursa ya kufanya mazoezi ya vitendo yaliyolenga kuimarisha uwezo wao wa kukabiliana na hali za dharura kwa ufanisi.

Programu hiyo ilitekelezwa kwa ushirikiano na mashirika mbalimbali ya ndani, ikiwemo Juhudi Mwenge Group, G4TC, British School, Kilimanjaro Institute, Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni, pamoja na WEO, No Limit Foundation, UDSM, Dingonet, TAYO na Sisi Tanzania. Kampuni ya Coca-Cola pia ilishiriki kwa kutoa vinywaji kwa washiriki kama sehemu ya msaada wake.

Mmoja wa washiriki alisema, “Kushiriki katika usafi wa mazingira na mafunzo ya usalama kumeongeza uelewa wangu kwamba amani inaweza kujengwa kupitia vitendo halisi katika jamii.”

Afisa mmoja wa IPYG alieleza kuwa shirika hilo litaendelea kupanua programu kama hizi kwa kushirikiana na wadau wa ndani ili kuimarisha ushiriki wa vijana katika ujenzi wa amani.







▪️ Watakiwa kuongeza bidii na kudumisha mshikamano

📍 Dodoma
WATUMISHI wa Tume ya Madini wameaswa kuzingatia weledi, uwajibikaji na mshikamano katika utekelezaji wa majukumu yao ili kuendeleza mafanikio ya Tume pamoja na kuongeza mchango wa sekta ya madini katika ukuaji wa uchumi wa taifa.

Akizungumza leo wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi) yaliyofanyika kimkoa katika Viwanja vya Jamhuri jijini Dodoma, Mkurugenzi wa Rasilimali Watu na Utawala wa Tume ya Madini, Nsajigwa Kabigi, amesema mafanikio yaliyopatikana yanapaswa kulindwa kwa kuongeza bidii, nidhamu na uwajibikaji kazini.

Kabigi amesema Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhani Lwamo, amewapongeza watumishi wote wa Tume waliopo Dodoma, wale walioshiriki maadhimisho ya kitaifa mkoani Njombe pamoja na watumishi waliopo katika mikoa mbalimbali ya kimadini nchini kwa juhudi zao katika kutekeleza majukumu ya kazi.

“Tumeaswa kuendelea kudumisha mshikamano, upendo na kufanya kazi kwa bidii ili kuendelea kuiweka Tume ya Madini katika nafasi ya juu ya utendaji,” amesema Kabigi.

Ameeleza kuwa Tume ya Madini imeendelea kufanya vizuri katika utekelezaji wa majukumu yake, akisisitiza kuwa ni wajibu wa kila mtumishi kuhakikisha taasisi inaendelea kuwa kinara katika ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali kutoka sekta ya madini.

Aidha, amesema waajiri wataendelea kulinda haki za wafanyakazi mahali pa kazi, huku akisisitiza kuwa watumishi wanapaswa kutekeleza majukumu yao kwa weledi, uadilifu na bidii ili kufikia malengo ya sekta ya madini na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.

Katika maadhimisho hayo ya Mei Mosi mkoani Dodoma, maandamano ya wafanyakazi yalianzia Viwanja vya Bunge na kuhitimishwa katika Viwanja vya Jamhuri, ambapo yalipokelewa rasmi na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule.




 Na Mwandishi Wetu.

Watumishi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) wakiwemo wa makao makuu na Kampasi ya Dar es Salaam, wameungana na wafanyakazi wengine kushiriki maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani ‘Mei Mosi’ 2026 yaliyofanyika kimkoa katika Viwanja vya Mnazi Mmoja Grounds, jijini Dar es Salaam.

Maadhimisho hayo yalihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali, sekta binafsi pamoja na mashirika ya umma, yakilenga kutambua mchango wa wafanyakazi katika maendeleo ya taifa na kujadili masuala ya ustawi wao mahali pa kazi.

Mgeni rasmi katika hafla hiyo alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, ambaye alitoa wito kwa wafanyakazi wote nchini kuzingatia uadilifu, uwajibikaji na nidhamu kazini ili kulinda taswira ya serikali.

Akizungumza mbele ya mamia ya wafanyakazi waliojitokeza kusherehekea siku hiyo, Chalamila alisema kuwa wafanyakazi ndio sura halisi ya serikali kwa wananchi, hivyo wanapaswa kutambua uzito wa nafasi walizonazo katika kuhudumia jamii.

“Tunaposherehekea siku hii muhimu, ni vyema tukatambua kuwa mfanyakazi mmoja anaweza kufanya serikali ipendwe au ichukiwe. Hivyo ni wajibu wa kila mtumishi kufanya kazi kwa uaminifu, bidii na kwa kuzingatia maadili ya utumishi wa umma,” alisema Chalamila.

Aliongeza kuwa serikali inaendelea kuthamini mchango wa wafanyakazi na itaendelea kuboresha mazingira ya kazi pamoja na maslahi yao ili kuongeza tija na ufanisi katika utoaji huduma kwa wananchi.

Kwa upande wao, watumishi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania walieleza kuwa ushiriki wao katika maadhimisho hayo ni sehemu ya kuonesha mshikamano na wafanyakazi wengine nchini pamoja na kuunga mkono juhudi za serikali katika kuboresha utumishi wa umma.

Maadhimisho ya Mei Mosi hufanyika kila mwaka duniani kote, yakilenga kuenzi mchango wa wafanyakazi na kuhamasisha haki, usawa na ustawi wao katika maeneo ya kazi.

Watumishi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kushiriki maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani ‘Mei Mosi’ 2026 yaliyofanyika kimkoa katika Viwanja vya Mnazi Mmoja Grounds, jijini Dar es Salaam.
Watumishi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania wakiwa katika ushiriki wa maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani ‘Mei Mosi’ 2026 yaliyofanyika kimkoa katika Viwanja vya Mnazi Mmoja Grounds, jijini Dar es Salaam.
Bw. Mussa Lugembe, Mkurugenzi wa Kampasi ya Dar es Salaam, akizungumza na watumishi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kwa niaba ya Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu. Picha zote na Emmanuel Massaka, Michuzi Tv.


Top News