DAR ES SALAAM, TANZANIA
KATIKA kuadhimisha miaka 78 ya Nakba (Janga la mwaka 1948), Ubalozi wa Dola ya Palestina nchini Tanzania jana tarehe 16 Mei 2026, uliandaa hafla maalum na ya kihistoria ya uonyeshaji wa filamu iliyoteuliwa kuwania tuzo za Oscar iitwayo "Palestine 36". Hafla hiyo kubwa ya kidiplomasia iliyofanyika jijini Dar es Salaam, iliongozwa na Mgeni Rasmi, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mheshimiwa Dkt. Ngwaru Jumanne Maghembe, na kuhudhuriwa na Mawaziri, Maafisa wa Serikali, Wajumbe wa Kundi la Wanadiplomasia (Diplomatic Corps), Mashirika ya Kimataifa, viongozi wa dini mbalimbali pamoja na wadau wa kijamii na vyombo vya habari.

Akihutubia hadhara hiyo, Balozi wa Dola ya Palestina nchini Tanzania, Mheshimiwa *Salam Abu Sharar*, alibainisha kuwa filamu hiyo si sanaa ya burudani tu, bali ni ushuhuda hai na chombo cha mapambano ya kuhifadhi kumbukumbu za mateso ya kihistoria dhidi ya jitihada za kufuta utambulisho wa Wapalestina. Balozi Abu Sharar alikumbusha ulimwengu juu ya maumivu yaliyorithiwa tangu mwaka 1948, ikiwemo mauaji ya kinyama ya Deir Yassin na kufukuzwa kwa nguvu kwa Wapalestina zaidi ya 750,000 kutoka kwenye ardhi zao. Alitoa wito mzito kwa jamii ya kimataifa kusimama kidete kutetea utu, kukataa kuhalalishwa kwa mifumo ya viwango viwili (double standards), na kuhakikisha sheria za kimataifa zinatumika kwa usawa ili kuwapatia Wapalestina haki yao ya msingi ya kuishi kwa uhuru na amani bila ukaliaji wa mabavu wa Israel.

Ubalozi wa Palestina unatoa shukrani zake za dhati kwa mshikamano huo mkubwa wa kidiplomasia. Balozi Salam Abu Sharar alieleza shukrani za kipekee kwa Serikali, wananchi, na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa msimamo wao thabiti na usioyeyuka katika kuunga mkono haki halisi za watu wa Palestina. Ubalozi ulisisitiza kuwa urafiki kati ya mataifa haya mawili si wa kiofisi tu, bali ni mwendelezo wa misingi imara ya kimaadili na ukombozi iliyoachwa na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, ambaye daima alisimama kidete dhidi ya ubeberu, ukoloni, na ubaguzi, akiamini kuwa uhuru na utu ni haki ya kila mwanadamu.




Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma .

Serikali imeendelea kuonesha dhamira yake ya kuboresha sekta ya usafirishaji wa bodaboda nchini kwa kuagiza halmashauri zote kutenga bajeti maalum kwa ajili ya ujenzi wa vituo na maegesho ya madereva wa pikipiki maarufu kama bodaboda.

Hatua hiyo inalenga kuboresha mazingira ya kazi kwa vijana wanaojishughulisha na huduma za usafirishaji pamoja na kuongeza ufanisi, usalama na utaratibu katika shughuli zao za kila siku.

Akijibu swali la Mbunge wa Bukoba Mjini, Eng. Johnston Johansen Mutasingwa, aliyehoji mpango wa Serikali wa kuwajengea vijana waendesha pikipiki maeneo rasmi ya maegesho, Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Dkt. Festo Dugange amesema Serikali tayari imeanza kuchukua hatua mbalimbali za kuboresha sekta hiyo muhimu ya ajira kwa vijana.

Dkt. Dugange amesema Serikali imezielekeza halmashauri zote nchini kuendelea kuwatambua madereva wa bodaboda na kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa vituo vyao katika maeneo mbalimbali.

Amesema hadi sasa Serikali imetenga maeneo 662 yenye ukubwa wa mita za mraba 5,859,756.18 katika halmashauri 146 nchini kwa ajili ya wafanyabiashara wadogo, wakiwemo madereva wa bodaboda.

Aidha, Serikali inaendelea na ujenzi wa ofisi za wafanyabiashara wadogo katika mikoa mbalimbali nchini ili kurahisisha usimamizi, mawasiliano na utekelezaji wa shughuli zao. Ofisi hizo pia zinatarajiwa kuwahusisha madereva wa bodaboda ili kuwapa mazingira bora ya kufanya kazi zao kwa uratibu zaidi.

Kwa mujibu wa Dkt. Dugange, kiasi cha shilingi milioni 260 tayari kimetolewa kwa ajili ya utekelezaji wa miradi hiyo katika mikoa 13 nchini.

Ameongeza kuwa baada ya kukamilika kwa utambuzi wa maeneo hayo na utoaji wa namba rasmi, Serikali itaendelea na ujenzi wa maegesho ya bodaboda katika vituo mbalimbali nchini, ikiwemo katika Manispaa ya Bukoba.

Hatua hiyo inaelezwa kuwa sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuwawezesha vijana kiuchumi kupitia sekta ya usafirishaji, huku ikiweka mazingira rafiki yatakayosaidia shughuli zao kufanyika kwa usalama, utaratibu na ufanisi zaidi.



Serikali imesema bado kuna watu wanaopinga mfumo wa stakabadhi za ghala kwa sababu zamani walikuwa wakinufaika kwa kuwanyonya wakulima kupitia biashara ya mazao, huku ikisisitiza kuwa mfumo huo umewekwa kwa lengo la kuhakikisha wakulima wanapata bei nzuri na faida halali ya mazao yao.

Hayo yameelezwa Mei 17, 2026 na Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dennis Londo, wakati akifungua uzinduzi wa maonesho ya maadhimisho ya miaka 20 ya mfumo wa stakabadhi za ghala yaliyofanyika Jijini Dodoma.

Ameeleza kuwa  mfumo huo umeendelea kuwa mkombozi kwa wakulima kwa kuwawezesha kuhifadhi mazao yao katika mazingira mazuri na kupata bei yenye ushindani tofauti na ilivyokuwa zamani ambapo baadhi ya wafanyabiashara walinunua mazao ya wakulima kwa bei ya chini iliyowapa hasara wakulima hao.

Londo amesema Serikali imeweka mazingira rafiki na wezeshi kupitia mfumo huo ili kuwasaidia wakulima kunufaika zaidi na mazao yao, huku baadhi ya watu wanaoupinga wakitaka kurejesha mazingira ya zamani yaliyokuwa yakiwanyima wakulima haki zao.

Aidha amesema kuwa, kilimo kinaendelea kuwa uti wa mgongo wa uchumi wa Taifa, hivyo Wizara ya Viwanda na Biashara imepewa jukumu la kuhakikisha wakulima wananufaika na mazao yao pamoja na kuongeza ushindani katika biashara ya mazao nchini.

Pia amesema katika kipindi cha uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, Serikali imeendelea kuimarisha mfumo wa stakabadhi za ghala ili kuchochea maendeleo ya sekta ya kilimo na kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050 ya kuifikisha Tanzania kwenye uchumi wa juu.

Amesema kuwa ushiriki wa sekta binafsi unatarajiwa kuchangia asilimia 70 kwenye ukuaji wa uchumi, huku akieleza kuwa ushirikiano wa taasisi zilizo chini ya Wizara za Viwanda na Biashara, Kilimo pamoja na Fedha umeendelea kuimarisha mfumo huo.

Hata hivyo, amesema Bodi ya Usimamizi wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala imeendelea kuwa mshirika muhimu katika kuimarisha ushindani wa biashara ya mazao nchini kwa kuongeza ushiriki wa sekta binafsi katika shughuli za ununuzi, huku ikiwawezesha wakulima kupata masoko ya uhakika na bei nzuri za mazao yao kupitia mfumo unaolenga kuongeza uwazi, tija na manufaa kwa wakulima.

Kwa upande wake, Witness Temba Afisa udhibiti ubora kutoka Bodi ya Usimamizi wa stakabadhi za Ghala, amesema katika kipindi cha miaka 20, Bodi hiyo imeendelea kutoa leseni kwa wadau mbalimbali wa biashara ya mazao na kuboresha uhifadhi wa mazao, jambo lililosaidia kupunguza upotevu wa mazao na kukuza uchumi wa wakulima.

Aidha, washiriki wa maonesho hayo wametakiwa kutumia fursa hiyo kubadilishana uzoefu na mawazo yatakayochangia utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 pamoja na kukuza uchumi wa Taifa kupitia sekta ya kilimo na biashara.



 

Kampuni ya mawasiliano ya Yas Tanzania imeendelea kuimarisha upatikanaji wa huduma za mawasiliano na kifedha nchini baada ya kuzindua rasmi duka jipya la Yas Store katika eneo la Kunduchi jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kampuni hiyo wa kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi na kuchochea maendeleo ya kidijitali kwa jamii.

Akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi huo iliyofanyika hivi karibuni, Mkurugenzi wa Huduma kwa Wateja na Uendeshaji wa Yas, Mwangaza Matotola, alisema kufunguliwa kwa duka hilo kutarahisisha upatikanaji wa huduma mbalimbali za Yas na Mixx kwa wakazi wa Kunduchi na maeneo ya jirani, hususan katika kipindi ambacho matumizi ya teknolojia yanaendelea kuongezeka kwa kasi nchini.

Alisema Kunduchi ni moja ya maeneo yanayokua kwa kasi kiuchumi na kijamii, huku wananchi wengi wakitegemea huduma za mawasiliano na kifedha katika shughuli zao za kila siku ikiwemo biashara, elimu na ajira za kujitegemea.

“Tunatambua umuhimu wa kuwafikia wananchi pale walipo. Kupitia duka hili, wateja wetu wataweza kupata huduma zote sehemu moja kwa urahisi zaidi,” alisema Matotola.

Aliongeza kuwa uwekezaji wa Yas katika miundombinu ya mawasiliano unaendelea kuleta matokeo chanya kwa Watanzania wengi, ambapo kampuni hiyo imewekeza zaidi ya trilioni moja katika kuboresha mtandao wake kote nchini, ikiwemo ujenzi wa minara zaidi ya 4,800 na upanuzi wa mtandao wa 4G na 5G unaowahudumia zaidi ya wateja milioni 31 nchini.

Kwa mujibu wa Matotola, uwekezaji huo umeendelea kufungua fursa mpya kwa vijana, wafanyabiashara na wanafunzi kwa kuwawezesha kupata huduma za kidijitali kwa urahisi zaidi na hivyo kuongeza ufanisi katika shughuli zao za kila siku.

“Teknolojia si anasa tena, ni sehemu muhimu ya maisha ya kila siku. Tunapoimarisha huduma za mawasiliano, tunasaidia biashara kukua, vijana kujiajiri kupitia majukwaa ya kidijitali, wanafunzi kupata elimu kwa urahisi zaidi na familia kuendelea kuwasiliana bila vikwazo,” alisisitiza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Uendeshaji wa Mixx, Arnold Ngarashi, alisema,

“Tunafahamu kuwa huduma za kifedha zimekuwa sehemu muhimu ya maisha ya kila siku ya wananchi wengi, kuanzia wafanyabiashara wadogo hadi vijana wanaojiajiri. Kupitia uwepo wa duka letu hapa Kunduchi, tumejipanga kurahisisha zaidi upatikanaji wa huduma za Mixx na kuwapa wananchi uwezo wa kufanya miamala yao kwa urahisi zaidi bila usumbufu,” alisema Ngarashi.

Aliongeza kuwa Mixx itaendelea kuhakikisha wananchi wanapata suluhisho za kidijitali zinazowasaidia kukuza biashara zao, kuweka akiba, kufanya malipo na kutuma fedha kwa urahisi zaidi, sambamba na kuchochea ujumuishi wa kifedha nchini.

Sambamba na hilo, Yas imewahimiza wananchi kutumia applikesheni mpya ya Yas App ambayo imezinduliwa hivi karibuni kwa lengo la kurahisisha upatikanaji wa huduma za kampuni hiyo kidijitali na kufurahia zawadi mbalimbali ndani ya App hiyo.

Wakazi wa Kunduchi waliohudhuria hafla hiyo walieleza kuwa ujio wa duka hilo utasaidia kupunguza changamoto ya kusafiri umbali mrefu kufuata huduma za mawasiliano na kifedha, huku wakiamini kuwa hatua hiyo itachochea shughuli za biashara na kuongeza urahisi wa upatikanaji wa huduma muhimu katika eneo hilo.

Kupitia upanuzi huo wa huduma, Yas na Mixx zinaendelea kuonesha dhamira yao ya kutumia teknolojia kama nyenzo ya kubadilisha maisha ya Watanzania na kuharakisha safari ya taifa kuelekea uchumi wa kidijitali.


Mkurugenzi wa Huduma kwa Wateja wa Yas Tanzania, Bi. Mwangaza Matotola (katikati), akikata utepe kuzindua rasmi duka jipya la Yas lililopo Kunduchi, Dar es Salaam, hivi karibuni. Wanaoshuhudia tukio hilo ni, kulia ni Mkuu wa Maduka wa Yas Tanzania, Bi. Sarah Sonelo pamoja na Mkuu wa kitengo cha Uendeshaji wa Huduma kwa Wateja, Bw. Henry Mboya (kushoto). Duka hilo jipya linalenga kuongeza upatikanaji wa huduma za kidijitali kwa wakazi na wafanyabiashara wa Kunduchi na maeneo ya jirani.

Benki ya NMB Plc imepata ufadhili wa jumla ya Dola za Marekani milioni 180, sawa na takribani Sh bilioni 468.1 za Kitanzania, kutoka IFC, British International Investment na Norfund, kwa ajili ya kuongeza mikopo kwa biashara ndogo na za kati, sekta ya kilimo, wanawake wajasiriamali na biashara zinazoongozwa na vijana nchini Tanzania.

Ufadhili huo unajumuisha Dola milioni 100 kutoka Shirika la Fedha la Kimataifa, IFC, sawa na takribani Sh bilioni 260; Dola milioni 50 kutoka British International Investment, BII, sawa na takribani Sh bilioni 130; na Dola milioni 30 kutoka Norfund, sawa na takribani Sh bilioni 78. Makubaliano hayo yalisainiwa jijini Kigali, Rwanda, pembezoni mwa Mkutano wa Wakurugenzi Wakuu Afrika, Africa CEO Forum.

Akizungumza wakati wa utiaji saini, Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu wa NMB, Ruth Zaipuna, alisema ufadhili huo ni ishara ya imani ya taasisi za kimataifa kwa mkakati wa NMB na nafasi yake katika kusaidia ukuaji wa uchumi wa Tanzania kupitia sekta binafsi, kilimo, wanawake na vijana.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji na Mkuu wa Kanda ya Afrika wa BII, Chris Chijiutomi, alisema uwekezaji huo unaendeleza ushirikiano wa muda mrefu kati ya BII na NMB, huku ukilenga kusaidia upatikanaji wa mitaji ya muda mrefu kwa MSMEs na biashara za kilimo. NMB inatarajiwa kutumia fedha hizo kuongeza mikopo, kuimarisha minyororo ya thamani ya kilimo na kupanua fursa kwa wajasiriamali nchini.
Hiii apa boss tumia.. Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu wa NMB Bank Plc, Ruth Zaipuna (kushoto), na Makamu wa Rais wa IFC Kanda ya Afrika, Ethiopis Tafara, wakionesha hati baada ya kusaini makubaliano ya ufadhili wa Dola za Marekani milioni 100 pembezoni mwa Mkutano wa Wakurugenzi Wakuu Afrika jijini Kigali, Rwanda. Ufadhili huo unatarajiwa kuongeza uwezo wa NMB kusaidia biashara ndogo na za kati, sekta ya kilimo na maeneo mengine muhimu ya uzalishaji nchini Tanzania.


Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu wa NMB Bank Plc, Ruth Zaipuna,Mkurugenzi Mtendaji na Mkuu wa Kanda ya Afrika wa BII, Chris Chijiutomi na Mkurugenzi wa Norfund Kanda ya Afrika Mashariki, William Nyaoke, wakibadilishana hati baada ya kusaini makubaliano ya ufadhili wa Dola za Marekani milioni 80 pembezoni mwa Mkutano wa Wakurugenzi Wakuu Afrika jijini Kigali, Rwanda. Ufadhili huo utasaidia kuongeza mikopo kwa SMEs, sekta ya kilimo na biashara ambazo hazijafikiwa kikamilifu nchini Tanzania.

Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu wa NMB Bank Plc, Ruth Zaipuna,Mkurugenzi Mtendaji na Mkuu wa Kanda ya Afrika wa BII, Chris Chijiutomi na Mkurugenzi wa Norfund Kanda ya Afrika Mashariki, William Nyaoke, wakisaini hati za makubaliano ya ufadhili wa Dola za Marekani milioni 80 pembezoni mwa Mkutano wa Wakurugenzi Wakuu Afrika jijini Kigali, Rwanda. Ufadhili huo utasaidia kuongeza mikopo kwa SMEs, sekta ya kilimo na biashara ambazo hazijafikiwa kikamilifu nchini Tanzania.












 

Na Mwandishi wetu- MBEYA

Serikali imeendelea kuimarisha uwezo wa Kitaifa wa Kuzuia, Kujiandaa, Kukabiliana na Kurejesha hali baada ya maafa ili kuhakikisha wananchi wanaishi katika mazingira salama ya  kuepuka madhara makubwa yatokanayo na maafa.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Tawala Msaidizi Mipango na Uratibu Ofisi ya Mkoa wa Mbeya, Dkt. Noah Sikwese wakati akifunga mafunzo kwa Wajumbe Wateule wa Timu ya Kukabiliana na Dharura (RERT), Waatalamu wa Unendeshaji wa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura (REOCC) katika Mkoa huo yaliyoandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa.

Dkt. Sikwese, amesema timu za kukabiliana na dharura zimejengewa msingi muhimu wa utendaji utakaowezesha Mkoa kuwa na uwezo wa kujiandaa na kukabiliana na matukio ya dharura kwa haraka  na ufanisi mkubwa .

“Timu hizi zitahusika katika kufanya tathmini za awali na za kina wakati wa maafa kubaini mahitaji halisi ya waathirika, pamoja na kuratibu upatikanaji wa rasilimali muhimu kwa ajili ya kukabiliana na athari za maafa,” alisema Dkt. Sikwese.

Pia, aliongeza kwamba mafunzo yamekuwa nyenzo muhimu katika kujenga na kuimarisha uwezo wa kitaalamu na kiutendaji kwa watumishi wanaohusika katika Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya dharura.

“Kuanzishwa kwa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura Mkoa wa Mbeya ni hatua muhimu katika kuimarisha uratibu wa shughuli za usimamizi wa maafa. Kituo hiki kitawezesha ufuatiliaji wa matukio  kwa ukaribu, ukusanyaji na uchambuzi wa taarifa kwa wakati, pamoja na kuimarisha mawasiliano miongoni mwa wadau,” alieleza.

Sambamba na hilo Dkt. Sikwese alifafanua kuwa, utekelezaji wa mafunzo hayo ulianza katika Mikoa a Mwanza, Arusha, Dodoma, ambapo hatua za kuanzisha Vituo vya Operesheni na Mawasiliano ya Dharura pamoja na kuimarisha Timu za kukabiliana  na maafa zilianza kutekelezwa.

“Ni matarajio yangu mafunzo haya yataongeza ufanisi, uwajibikaji, ustahimilivu dhidi ya majanga katika Mkoa wetu wa Mbeya,”aliongeza.

Aidha, alitoa wito kwa wataalamu wote waliopatiwa mafunzo kuendelea kuyafanyia kazi maarifa na stadi, kudumisha nidhamu ya kazi na kujenga utamaduani wa ushirikiano wa kitaalamu huku akiwasisitiza kuendelea kufanya mazoezi ya mara kwa mara ya uokoaji na  utoaji wa huduma ya kwanza kwa majeruhi au waliofikwa na maafa.

“Usimamizi wa maafa ni jukumu letu sote, kila mmoja ashiriki sasa na kuchukua hatua katika eneo lake ili kuokoa na kulinda maisha, mali na mazingira,” alisisitiza Dkt. Sikwese.

Ikumbukwe kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) kwa mujibu wa Sera ya Taifa ya Usimamizi wa Maafa yam waka 2004 (Toleo la 2025) pamoja na Sheria ya Usimamizi wa Maafa Na. 6 ya mwaka 202 imeipa jukumu la kuratibu masuala yote ya usimamizi wa maafa nchini.





Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) umeendelea kuonesha dhamira yake ya kupunguza pengo la kidijitali nchini kwa kutekeleza miradi mbalimbali inayolenga kuongeza upatikanaji wa huduma za mawasiliano, intaneti na kuwajengea uwezo wananchi, hususan wasichana na vijana, katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).

Hayo yameelezwa na Kaimu Mtendaji Mkuu wa UCSAF, Mhandisi Albert Richard, wakati akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya mfuko huo katika semina iliyowakutanisha waandishi wa habari na wahariri jijini Dodoma.

Akizungumza katika semina hiyo, Mhandisi Richard amesema UCSAF imefanikiwa kuwajengea uwezo wanafunzi 1,300 wa kike kutoka shule za sekondari za umma kupitia maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Msichana na TEHAMA (Girls in ICT Day), ambayo huadhimishwa kila mwaka mwezi Aprili.

Amesema kupitia maadhimisho hayo, wanafunzi hupatiwa mafunzo kuhusu matumizi sahihi ya TEHAMA, ubunifu wa kidijitali pamoja na fursa mbalimbali zilizopo katika sekta ya teknolojia, hatua inayolenga kuwahamasisha wasichana kujikita katika masomo na taaluma zinazohusiana na sayansi, teknolojia na mawasiliano.

“Lengo letu ni kupunguza pengo la ushiriki lililopo kati ya wasichana na wavulana katika sekta ya TEHAMA na kuhakikisha wasichana wanapata nafasi sawa katika ulimwengu wa kidijitali,” amesema Mhandisi Richard.

Amefafanua kuwa katika mwaka wa fedha 2025/2026, UCSAF kwa kushirikiana na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), ilifanikiwa kutoa mafunzo ya TEHAMA kwa jumla ya wasichana 440, wakiwemo wanafunzi wa shule za msingi, sekondari, vyuo, elimu ya awali pamoja na wenye ulemavu.

Mafunzo hayo yalitolewa katika vituo vya Arusha, Dar es Salaam, Dodoma, Mbeya na Zanzibar, huku yakilenga kuongeza uelewa wa matumizi ya teknolojia na kuwapa washiriki ujasiri wa kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kidijitali.

Mbali na uwezeshaji wa vijana, UCSAF pia inaendelea na utekelezaji wa mradi wa kutoa huduma za bure za intaneti katika maeneo ya wazi yenye matumizi makubwa ya wananchi, ikiwa ni sehemu ya kuongeza upatikanaji wa huduma za kidijitali kwa urahisi zaidi.

Kupitia mradi huo, vituo 17 vya intaneti ya bure vimeanzishwa katika Viwanja vya Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Sabasaba jijini Dar es Salaam. Aidha, huduma hiyo imefikishwa katika maeneo mbalimbali ikiwemo Nyerere Square na Chuo cha Informatics CIVE jijini Dodoma, Soko la Nyamagana jijini Mwanza, Kiembesamaki Zanzibar, Soko la Tabora pamoja na Lungemba Training College iliyopo Mafinga.

Kwa mujibu wa Mhandisi Richard, katika mwaka wa fedha 2024/2025 UCSAF pia ilitekeleza mradi wa intaneti ya bure katika vituo 25 vya mabasi ya mwendokasi (BRT-DART) kwa gharama ya shilingi milioni 500.

Amesema kwa mwaka wa fedha 2025/2026, utekelezaji wa mradi huo unaendelea katika maeneo 60 ya Tanzania Bara na Zanzibar, ikiwa ni jitihada za kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanapata huduma za intaneti kwa urahisi na gharama nafuu.

Katika hatua nyingine, UCSAF inaendelea kutekeleza mradi wa kuunganisha ofisi za halmashauri na mkongo wa taifa wa mawasiliano kwa njia ya faiba ili kuboresha huduma za intaneti katika taasisi za umma.

Mhandisi Richard amesema tayari utambuzi wa maeneo 10 umekamilika, huku mchakato wa manunuzi ukiendelea ili kumpata mkandarasi atakayetekeleza kazi ya kuunganisha huduma hizo pamoja na kujenga miundombinu ya kufikisha faiba katika maeneo husika.

Sambamba na hilo, UCSAF inaendelea na mradi wa kuongeza uwezo wa minara 62 ya mawasiliano kutoka teknolojia ya 2G kwenda 3G na 4G, hatua inayolenga kuboresha huduma za mawasiliano na intaneti katika maeneo ya vijijini.

Amesema kati ya minara hiyo, minara 37 inatekelezwa na kampuni ya Vodacom ambapo tayari imekamilika na imeanza kutoa huduma ya intaneti yenye kasi, huku minara 25 inayotekelezwa na TTCL ikiwa katika hatua za awali za manunuzi.

Kwa mujibu wa UCSAF, utekelezaji wa miradi hiyo unalenga kuongeza uwezo wa wananchi kupata huduma bora za mawasiliano, kukuza matumizi ya huduma za kidijitali na kuchochea shughuli za kijamii na kiuchumi kupitia teknolojia.

Aidha, miradi hiyo inatarajiwa kusaidia kuboresha huduma muhimu kama elimu mtandao, afya mtandao, biashara mtandao pamoja na huduma za kifedha kupitia simu za mkononi, hasa kwa wananchi wa maeneo ya vijijini na yasiyokuwa na huduma bora za mawasiliano.






▪️ Asema utekelezaji wa Bwawa la Farkwa kuanza baada ya kukamilika kwa taratibu za manunuzi

▪️ Aagiza kukomeshwa kwa ukamataji usio na msingi wa vitendea kazi vya wananchi

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali imejipanga kuhakikisha miradi yote ya maendeleo iliyopungua kasi ya utekelezaji inaanza tena kutekelezwa kwa kasi inayotakiwa ili wananchi waendelee kunufaika na huduma za kijamii na kiuchumi.

Amesema hayo leo Jumapili, Mei 17, 2026, alipowahutubia wananchi wa Wilaya ya Chemba katika Viwanja vya Shule ya Msingi Kambi ya Nyasa, akiwa katika ziara ya kusikiliza na kutatua changamoto za wananchi.

Dkt. Mwigulu amesema baadhi ya miradi ilipungua kasi baada ya Serikali kuelekeza nguvu kubwa katika kukamilisha miradi ya kimkakati ya kitaifa iliyokuwa imefikia hatua za mwisho, ikiwemo Mradi wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere, reli ya kisasa pamoja na Daraja la Kigongo–Busisi.

“Kilichosababisha baadhi ya miradi kupungua kasi haikuwa uzembe wala kupuuza. Ilikuwa ni mkakati wa kukamilisha miradi iliyokuwa imekaribia kukamilika ili ianze kutumika,” amesema.

Amesema Serikali sasa imeweka kipaumbele katika kuhakikisha miradi yote iliyokuwa imepungua kasi inaanza tena kutekelezwa, huku miradi ambayo mikataba yake tayari imesainiwa ikitengewa fedha za kuanza kazi.

Kuhusu Mradi wa Bwawa la Farkwa, Dkt. Mwigulu amesema mradi huo, unaokadiriwa kugharimu zaidi ya shilingi bilioni 312, utaanza kutekelezwa mara baada ya kukamilika kwa taratibu za kimanunuzi.

“Tunapoanza bajeti mpya naamini mtakuwa mmeanza kuona mkandarasi akiwa eneo la mradi kutekeleza mradi huo wa kihistoria,” amesema.

Amesema Serikali imeelekeza miradi mipya ya maji ibuniwe kwa namna itakayotoa huduma ya maji kwa matumizi ya nyumbani, mifugo na shughuli za kilimo.

Aidha, Dkt. Mwigulu amesema Serikali imeendelea kufanya uwekezaji mkubwa katika sekta za afya, elimu, maji na nishati, hatua ambayo imebadili kwa kiwango kikubwa maisha ya wananchi.

Katika sekta ya afya, amesema Serikali imejenga hospitali za wilaya zaidi ya 100, vituo vya afya zaidi ya 600 na zahanati zaidi ya 2,700, sambamba na ununuzi wa vifaa tiba vya kisasa vya uchunguzi katika hospitali za rufaa na za kanda.

Katika sekta ya elimu, amesema Serikali imejenga shule za amali 103, zikiwemo shule 29 za mkondo wa uhandisi, pamoja na kuendelea kuongeza miundombinu ya shule za msingi na sekondari nchini.

Kuhusu nishati, Dkt. Mwigulu amesema Serikali imejipanga kumaliza changamoto ya kukatika kwa umeme kupitia utekelezaji wa Mradi wa Gridi Imara wenye thamani ya zaidi ya shilingi trilioni 1.1.

“Mkiona umeme unakatika katika baadhi ya maeneo siyo upungufu wa umeme tena. Changamoto ipo kwenye uimara wa gridi kutokana na ongezeko kubwa la matumizi,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameagiza viongozi na watendaji kuacha vitendo vya ukamataji usio na msingi pamoja na kushikilia vitendea kazi vya wananchi kwa makosa madogo.

“Haya mambo ya kushikilia vitendea kazi vya wananchi tuachane nayo. Mtu anafanya shughuli yake ya kujitafutia kipato halafu mnachukua kitendea kazi chake; hiyo ni kuua mtaji na maisha ya familia yake,” amesema.

Amesema Serikali itaendelea kulinda haki za wananchi na kuhakikisha sheria hazitumiki kuwaonea wananchi au kuwanyima fursa za kufanya shughuli halali za uzalishaji.

Aidha, amesema Serikali inaendelea na hatua za kuifuta sheria ya kutaifisha mali ambayo imekuwa ikitumika vibaya katika baadhi ya maeneo na kusababisha wananchi kupoteza mali zao isivyo halali.








Na Mwandishi wetu – Dar es Salaam

Serikali imeeleza hazma yake ya kuendelea kutekeleza miradi ya mashirikiano katika sekta za kilimo na Uvuvi kwa pande mbili za Muungano ili kuongeza Ajira, uzalishaji mali, kuboresha usalama wa chakula, kuongeza thamani ya mazao, na kukuza Uchumi wa Buluu.

Hayo yameelezwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu Profesa Palamagamba Kabudi katika kikao cha ngazi ya Mawaziri cha Mashirikiano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kilichofanyika katika Ukumbi wa Mkutano wa Ofisi ya Waziri Mkuu Mtaa wa Magogoni Jijini Dar es Saalaam leo Tarehe 17 Mei 2026.

Azingumzia Programu ya kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) inayotekelezwa na pande zote Mbili za Muungano, Profesa Kabudi amesema Serikali itaimarisha ushiriki katika sekta ya uvuvi wa Bahari kuu kwa kuwezesha mashirika ya uvuvi (TAFICO) kwa Tanzania Bara na (ZAFICO) kwa upande wa Zanzibar kwa kuwezeshwa kujenga meli sita za uvuvi sambamba na ujenzi wa viwanda vya kuchakata Samaki ambapo kwa upande wa Tanzania Bara kiwanda hicho kitajengwa katika wilaya ya Kilwa Mkoani Lindi na Zanzibar katika eneo la Fungurefu.

Aidha, kwa upande wa Utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi alisema kuwa, Serikali imejiandaa kutoa taarifa ya Utekelezaji wa Ilani ya chama hicho ya nusu mwaka kwa pande zote mbili za Muungano ifikapo mwezi Julai, 2026 na taarifa ya mwaka mzima ifikapo mwezi Novemba 2026.

Kwa upande wake Waziri wa Nchi, Ofisi wa Makamu wa Pili wa Rais anayeshughulikia masuala ya Sera, Uratibu na Baraza la Wawakilishi Mhe. Hamza Hassan Juma alisema Watanzania wengi wanajishughulisha na masuala ya kilimo hivyo kikao hicho kimeweza kuzungumzia fursa zinazopatikana katika sekta hizo zinazoratibiwa na ofisi hizo na kuongeza kuwa mafanikio mengi yanategemewa kupatikana katika vikao hivi vya mashirikiano.











Top News