Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Mlezi wa Mtandao wa Wanawake Viongozi Afrika (AWLN) Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Liberia Mhe. Ellen Johnson Sirleaf mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 20 Aprili, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Mwanachama wa Mtandao wa Wanawake Viongozi Afrika (AWLN) Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Shirikisho la Kidemokrasia la Ethiopia Mhe. Sahle - Worke Zewde mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 20 Aprili, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Uongozi wa Mtandao wa Wanawake Viongozi Afrika (AWLN) uliongozwa na Mlezi wake Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Liberia Mhe. Ellen Johnson Sirleaf, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 20 Aprili, 2026.







Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza jambo na Mlezi wa Mtandao wa Wanawake Viongozi Afrika (AWLN) Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Liberia Mhe. Ellen Johnson Sirleaf pamoja na Mwanachama wa Mtandao huo, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Shirikisho la Kidemokrasia la Ethiopia Mhe. Sahle - Worke Zewde mara baada ya mazungumzo yao, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Aprili, 2026.






 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Uongozi wa Mtandao wa Wanawake Viongozi Afrika (AWLN), uliongozwa na Mlezi wake Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Liberia Mhe. Ellen Johnson Sirleaf pamoja na Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Shirikisho la Kidemokrasia la Ethiopia Mhe. Sahle - Worke Zewde, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Aprili, 2026.






Na Karama Kenyunko Michuzi Tv 

MWANAMKE  Monica Beda (36), mkazi wa Kimara jijini Dar es Salaam amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na shtaka la kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu kiasi cha shilingi milioni 60.

Katika hati ya mashtaka iliyosomwa mahakamani hapo leo Aprili 20,1026 na Wakili wa Serikali Cathbert Mbiling’i  imeileza mahakama kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo Novemba 8, 2025, katika Mtaa wa Samora, jijini Dar es Salaam.

Mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu Salome Mshasha, imedaiwa mshtakiwa alimlaghai Agrey Festo Mashanda kwa kujifanya angeweza kumuagizia gari aina ya Mitsubishi Fuso Fighter Damper lenye chassis namba  FK418F-550031, huku akijua kuwa si kweli.

Kwa mujibu wa upande wa mashtaka  upelelezi wa shauri hilo umekamilika na wameomba kupangiwa tarehe kwa ajili ya usikilizwaji wa awali (PH).

Hata hivyo mshtakiwa amekana kutenda kosa hilo na amerudishwa rumande kwa kushindwa kutimiza masharti ya dhamana 

Mahakama ilimpatia mshtakiwa dhamana kwa masharti ya kuwa na wadhamini wawili wa kuaminika, ambapo mmoja wao anatakiwa kuwasilisha hati ya mali isiyohamishika au fedha taslimu yenye thamani ya nusu ya fedha anazodaiwa kuiba, sawa na shilingi milioni 30.

Kesi hiyo limeahirishwa hadi Mei 6, 2026 kwa ajili ya mshtakiwa kusomewa maelezo ya awali.



Na Said Mwishehe,Michuzi TV

JUBILEE Health Insurance imetoa elimu kuhusu afya ya akili kwa wanafunzi wa Shule ya Sekondari Mzizima jijini Dar es Salaam lengo likiwa kuijengea uelewa jamii kuhusu afya ya akili huku ikieleza mpango huo utafanyika kwa wanafunzi wa shule mbalimbali nchini.

Akizungumza katika Shule ya Sekondari Mzizima jijini Dar es Salaam wakati wa kutolewa elimu kuhusu afya ya akili kwa wanafunzi 100 wa shule hiyo , Dk.Milembe Makoye ambaye ni Senior wellness officer kutoka Jubilee Health Insurance amesema wanaamini elimu ni ufunguo wa maisha hivyo wakielewa watajitambua.

“Tuko hapa kwa ajili ya kutoa elimu kuhusiana na afya ya akili lakini afya kwa ujumla.Kwanini tumeamua kutoa elimu hii ? Tunaamini wakielewa watajitambua.

“Kwanini afya ya akili ? Afya ya akili ni jambo ambalo ni changamoto kwa watu wengi sio kwa watu wazima pekee, lakini hata kwa watoto ambao wamekuwa wanasahaulika.

“Sasa kama Jubilee Health Insurance tunaamua kuingia kwenye jamii kuwagusa watoto wapate elimu sahihi waweze kujitambua ili hata wanapokua waweze kudhibiti changamoto ya matatizo ya afya ya akili lakini na afya ya mwili kwa ujumla,”amesema Dk.Makoye.

Aidha amesema Sekondari ya Mzizima ni ya kwanza kufikiwa lakini watakwenda shule nyingi zaidi kadri watakavyoweza huku akifafanua sababu za kuja na programu hiyo inatokana na ukweli Jubilee Health Insurance wanatoa huduma za bima ya afya.

“Lakini tukaona tusiishie kutoa tu bima basi tuguse jamii kwa kutoa elimu ya ustawi wa Afya, maana wakielewa maana ya afya ya akili watachukua njia sahihi ya kutunza afya zao na hapo tutakuwa tumefuzu.

Kwa upande wake Dkt.Isaac Marro akizungumza baada ya kutoa elimu ya afya ya akili kwa wanafunzi hao amesema kuna kila sababu ya Jamii kuwa na uelewa na afya ya akili mapema kwani kwa muda mrefu elimu kuhusu changamoto ya akili inatolewa kwa watu wazima.

“Kwa kifupi afya ya akili duniani kote imekuwa changamoto kubwa lakini tofauti na wenzetu ambao wao mapema waliwahi kubaini sisi tukachelewa.Kwahiyo changamoto zilipoanza kuwa kubwa na mapokeo yameendelea kuwa hasi.

Amesisitiza umuhimu kuzungumza kuhusu afya ya akili kuanzia umri mdogo wakiwemo watoto na vijana ili wajue, kwani hiyo inasaidia kutengeneza sio tu mbinu za kujilinda lakini pia kujilinda wenyewe kwa wenyewe.

Wakati huo huo Mshauri wa wanafunzi katika Sekondari ya Mzizima Theresia Mwaijala ametoa pongezi kwa Jubilee Health Insurance kwa kuona umuhimu wa kutoa elimu ya afya ya akili kwa wanafunzi.

“Juhudi zinazofanywa na Jubilee Health Insurance ni nzuri, wamekuja shuleni kwetu kuzungumza na wanafunzi kuhusu afya ya akili kitu ambacho ni muhimu kwasababu tunafahamu changamoto ya afya ya akili zinaanza mapema kuanzia miaka 14.

Hivyo amesema vizuri watoto wakapewa uelewa ,wafundishwe ili waweze kujilinda lakini wakiona kama kuna dalili ambazo zinaweza kusababisha afya ya akili wachukue hatua

Amesisitiza mafunzo ya Jubilee Health Insurance kuhusu afya ya akili kwa ujumla yanafaida kubwa ikiwemo kupata uelewa, na ukiwa na uelewa utachukua hatua sahihi.”



Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Waziri katika Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana, Joel Nanauka, amesema kuwa katika mwaka wa fedha 2026/2027, serikali itatekeleza mpango wake kwa kuzingatia vipaumbele vinne vikuu vinavyolenga kuimarisha maendeleo ya vijana nchini.

Akizungumza leo bungeni mjini Dodoma wakati akiwasilisha mpango na makadirio ya matumizi ya Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana, Nanauka alisema lengo kubwa la vipaumbele hivyo ni kuwawezesha vijana kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi, kijamii na kisiasa, pamoja na kuboresha ustawi wao kwa ujumla.

Kwa mujibu wa Nanauka, vipaumbele hivyo vitajikita katika maeneo yafuatayo:

Kwanza, kuimarisha ukuzaji wa biashara na uwezeshaji wa vijana kiuchumi, kwa lengo la kuwasaidia vijana wengi zaidi kujiajiri na kuajiriwa katika sekta za biashara na uzalishaji.

Pili, kuimarisha uratibu na ushirikishwaji wa vijana katika masuala ya kijamii, kiuchumi na kisiasa ili kuongeza ushiriki wao katika maendeleo ya taifa.

Tatu, kuimarisha uratibu wa elimu ya uraia, uzalendo pamoja na usimamizi wa shughuli za Mwenge wa Uhuru nchini.

Nne, kuimarisha ustawi na makuzi bora ya vijana ili kuhakikisha wanakua katika mazingira yanayowawezesha kufikia ndoto zao na kuchangia maendeleo ya taifa.

Nanauka alisisitiza kuwa mpango huo ni sehemu ya juhudi za serikali kuhakikisha vijana wanakuwa nguzo muhimu ya maendeleo ya taifa kupitia fursa za kiuchumi na ushiriki mpana katika ujenzi wa nchi.



Na Janeth Raphael

Serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo imesema kuwa mpango wa mkopo wa shilingi bilioni 20 uliotengwa kwa ajili ya kuwawezesha watengenezaji wa maudhui mitandaoni (content creators) umeonyesha mwitikio mkubwa kuliko ilivyotarajiwa, hali inayoashiria ongezeko kubwa la vijana wanaojihusisha na sekta ya ubunifu wa kidigitali nchini.

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya utiaji saini wa makubaliano ya Tanzania kuwa mwenyeji wa Mashindano ya 74 ya Miss World 2027, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, amesema lengo la mkopo huo ni kuwawezesha vijana wenye vipaji lakini wenye changamoto za kifedha ili waweze kukuza ubunifu wao na kujiajiri kupitia maudhui ya kidigitali.

Makonda amesema mpango huo ulipangwa kwa nia ya kuwasaidia vijana wanaoanza safari yao ya ubunifu, hasa wale wanaokosa vifaa muhimu kama kamera bora, vifaa vya uhariri, na rasilimali nyingine za msingi zinazohitajika katika uzalishaji wa maudhui ya kisasa.

Hata hivyo, amesema tathmini ya awali imeonesha kuwa maombi yamezidi kiwango kilichotarajiwa, jambo linaloonesha wazi kuwa sekta ya content creation imekuwa na mvuto mkubwa na inakua kwa kasi nchini Tanzania.

“Hatuwezi kuchukua mkopo huu tukawapa watu ambao tayari wana uwezo mkubwa, kama kumiliki magari ya gharama kubwa au kuwa na vifaa vya kisasa. Dhamira yetu ni kumsaidia kijana wa kawaida aliye mtaani, mwenye ndoto lakini hana uwezo wa kuanza,” amesema Makonda.

Kutokana na hali hiyo, Waziri huyo amesema serikali imeamua kuahirisha kwa muda utekelezaji wa mpango huo ili kufanya maboresho muhimu, yakiwemo marekebisho ya vigezo na masharti ya mkopo huo ili kuhakikisha unawafikia walengwa sahihi.

Ameongeza kuwa maboresho hayo yatalenga pia kuweka riba nafuu na masharti rahisi zaidi ili kuhakikisha mkopo huo hauwi mzigo kwa vijana, bali unakuwa kichocheo cha ukuaji wa sekta ya ubunifu na ajira nchini.

Serikali imesisitiza kuwa dhamira yake ni kuhakikisha vijana wengi zaidi wananufaika na fursa zilizopo kwenye uchumi wa kidigitali, ambao kwa sasa unaendelea kukua kwa kasi na kutoa nafasi kubwa za ajira na ubunifu.


Na Janeth Raphael- MichuziTv -Dodoma .

Serikali imetangaza mpango wa kuanzisha utafiti maalum utakaoweka msingi wa uanzishwaji wa Benki ya Vijana, hatua inayolenga kuboresha upatikanaji wa huduma za kifedha kwa vijana na kuondoa changamoto zinazowakabili katika kupata mikopo na mitaji ya biashara.

Akizungumza Bungeni jijini Dodoma leo Jumatatu, wakati akiwasilisha makadirio ya bajeti ya Wizara ya Maendeleo ya Vijana kwa mwaka wa fedha 2026/27, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais anayeshughulikia vijana, Mhe. Joel Nanauka, amesema utafiti huo utaanza rasmi katika mwaka huo wa fedha.

Amesema lengo kuu ni kubaini muundo sahihi wa taasisi hiyo ya kifedha ambayo itakuwa maalum kwa vijana, ili kuhakikisha inazingatia mazingira yao, uwezo wao wa kiuchumi na mahitaji halisi ya soko la ajira na uwekezaji.

Kwa mujibu wa Waziri Nanauka, Benki ya Vijana itakuwa chombo cha kimkakati kitakachosaidia kukuza ubunifu katika huduma za kifedha, kuongeza fursa za uwekezaji kwa vijana na kuchochea ajira mpya nchini. Pia, itasaidia kujenga mfumo imara wa kifedha unaojumuisha makundi yote ya vijana bila vikwazo vya kimtaji.

Aidha, serikali imeeleza kuwa itaendelea kuimarisha programu za mafunzo ya ujasiriamali na usimamizi wa biashara kwa vijana, sambamba na kuongeza upatikanaji wa mikopo nafuu kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Vijana ili kuwawezesha kujiajiri na kuajiri wengine.

Katika hatua nyingine, Waziri huyo amesema serikali pia inapanga kufanya utafiti wa kuanzisha Vituo vya Ubunifu kwa Vijana (Youth Innovation Hubs) vitakavyolenga kukuza vipaji, ubunifu na mawazo ya kibiashara. Vituo hivyo vitakuwa kiunganishi kati ya vijana na masoko, teknolojia pamoja na mitaji.

Pia, serikali itakuja na mfumo wa kitaifa wa kuratibu masuala ya maendeleo ya vijana pamoja na kuanzisha kanzidata ya taifa itakayokusanya taarifa muhimu za vijana ili kusaidia kupanga na kutekeleza sera kwa ufanisi zaidi.

Vilevile, mapitio ya sheria ya Baraza la Vijana yanatarajiwa kufanyika ili kuliboresha zaidi katika kusimamia na kuwakilisha maslahi ya vijana nchini.

Serikali imeeleza kuwa hatua hizi zote zinalenga kuongeza ushiriki wa vijana katika uchumi na kuhakikisha wanakuwa sehemu muhimu ya maendeleo ya taifa kupitia mfumo jumuishi wa kiuchumi na kijamii.


Serengeti. Serengeti Premium Apple imeandika historia kwa kuwasilisha uzinduzi wa kipekee ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, ikiweka alama kama kinywaji premium (RTD) cha kwanza kutengenezwa Tanzania na kampuni ya Serengeti Breweries Limited (SBL).

Kupitia matukio ya uzinduzi kwa siku tatu mfululizo, zaidi ya mastaa na watengeneza maudhui 30 kutoka sekta mbalimbali za ubunifu walisafirishwa kwa ndege binafsi kutoka Dar es Salaam mpaka Serengeti, wakipata fursa ya kushiriki na kufurahia matukio ya kipekee yaliyounganisha na ladha laini na ya kuburudisha ya kinywaji hicho, utamaduni na mandhari ya asili ya Tanzania.

Safari hiyo ilijumuisha matukio mbalimbali yaliyopangiliwa kwa ustadi na ubunifu, kuanzia mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, safari ya ndege binafsi angani, mpaka mapokezi ya kipekee ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti. Mastaa hao walipata nafasi ya kushiriki shughuli kama vile kutembelea na kujionea mbuga, chakula cha mchana (brunch) na cha jioni (dinner) katika mazingira ya kuvutia kilichoambatana na tafrija fupi. 

Siku iliyofuatia walishiriki kwa pamoja tukio la kipekee la “Toast in the Sky” lililofanyika kupitia ‘hot air balloon’ juu ya anga la Serengeti. Wageni waalikwa waliandaliwa shughuli tofauti zinazoonyesha namna kinywaji hiki kipya kinavyoweza kuakisi ubora na maisha ya kisasa yenye hadhi ya kimataifa.

Uzinduzi huu uliakisi kwa vitendo misingi mikuu ya chapa mpya ya Serengeti Premium Apple, ikiwemo ladha laini na ya kuburudisha ya apple; fahari ya bidhaa ya Kitanzania inayowakilisha ubunifu, usasa na mafanikio ya Mtanzania wa kisasa; pamoja na kuhamasisha Watanzanie kuendele kuvumbua na kufurahia uzuri na maeneo mapya nchini, ladha mpya na mtazamo mpya wa maisha.

Kupitia uzinduzi huu, kampuni ya Serengeti Breweries Limited imeonyesha uwezo wa Tanzania kutengeneza bidhaa zinazokidhi viwango vya kimataifa huku ikitumia utajiri wa rasilimali zilizopo kama jukwaa la kuonesha ubunifu na hadhi ya juu.






































Waziri wa Fedha Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akichangia mada katika mkutano ulioangazia umuhimu wa sekta ya maji katika maendeleo ya watu na uchumi wa dunia, chini ya kauli mbiu “usalama wa maji kwa mustakabali wa bara la Afrika: mtazamo wa mbele” ulioandaliwa na Benki ya Dunia, pembezoni mwa mikutano ya majira ya Kipupwe ya Benki hiyo na Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF, uliofanyika jijini Washington D.C, nchini Marekani.
(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Washington D.C, Marekani)

Na Benny Mwaipaja, Washington D.C
WAZIRI wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amesisitiza umuhimu wa nchi za Afrika kuweka mipango ya kuhakikisha kuwa maji salama yanapatikana kwa ajili ya matumizi ya binadamu na shughuli za kiuchumi lakini pia kulinda vyanzo vya maji.

Mhe. Balozi Omar alisema hayo wakati akichangia mada katika mkutano ulioangazia umuhimu wa sekta ya maji katika maendeleo ya watu na uchumi wa dunia, chini ya kauli mbiu “usalama wa maji kwa mustakabali wa bara la Afrika: mtazamo wa mbele” ulioandaliwa na Benki ya Dunia, pembezoni mwa mikutano ya majira ya Kipupwe ya Benki hiyo na Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF, uliofanyika jijini Washington D.C, nchini Marekani.

Akijibu swali la namna rasilimali za maji zinavyoweza kulindwa na kutumika kama rasilimali za kiuchumi, Mhe. Balozi Omar alisema ni muhimu ieleweke kwamba maji ni rasilimali muhimu hivyo ni lazima kufanya utafiti wa kutambua vyanzo vya maji vilivyopo ikiwemo mito na maziwa na kuweka utekelezaji wake kwenye mipango ya kitaifa ya maendeleo ya muda mfupi, wa kati na muda mrefu.

“Pia ni muhimu kuvifuatilia na kuvilinda vyanzo hivyo na kuzitumia rasilimali hizo kwa uangalifu mkubwa ili tuendelee kuwa na maji safi, kuvilinda vyanzo hivyo dhidi ya uvamizi na uchafuzi wa maji, pamoja na kuondoa upotevu wa maji.” Alisema Mhe. Balozi Omar

Alitahadharisha kuwa idadi ya watu inaendelea kuongeza kwa kasi barani Afrika hatua iliyosababisha kuwa na uhitaji mkubwa wa maji na kushauri kuwepo kwa ushirikiano madhubuti kati ya sekta binafsi na wadau wengine wa maendeleo kama Benki ya Dunia ili kuwezesha upatikanaji wa rasilimali fedha kwa ajili kutekeleza mira ya maji.

Mkutano huo wa maji uliwashirikisha Mawaziri wa Fedha na wadau wengine kutoka nchi wanachama wa Benki ya Dunia kutoka baadhi ya nchi za Bara la Afrika ambapo walijadili namna sera, uwekezaji, mabadiliko ya kimfumo wa kitaasisi unavyoweza kuboresha na kuongeza upatikanaji wa maji safi na salama barani Afrika.



Na Mwamvua Mwinyi, Chalinze, Aprili 19, 2026
MWENGE wa Uhuru umetambua mchango wa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora,ambae pia ni Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete, kufuatia kuandika kitabu(andiko) kinachoelezea falsafa ya Mwenge wa Uhuru tangu kuanzishwa kwake mwaka 1961.

Imeelezwa Juhudi hizo za Ridhiwani, amezifanya wakati alipokuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, kuandika andiko hilo rasmi Kiserikali.

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026, Wazo Mwang’onda, alitambua mchango huo kuwa sehemu ya historia ya Taifa wakati wa mapokezi ya Mwenge wa Uhuru yaliyofanyika Aprili 19, 2026 katika Shule ya Msingi Kiwangwa, Halmashauri ya Chalinze, ukitokea Halmashauri ya Bagamoyo.

Mbali ya hilo, Ridhiwani ametajwa kuwa miongoni mwa wananchi wawili wa wilayani Bagamoyo waliotoa mchango wa kipekee kwa jamii, ambapo mmoja alijitolea kuvusha watoto darajani kwenda shule, huku mwingine akitoa eneo kwa ajili ya ujenzi wa shule.

Mwang'onda alieleza, Mwenge wa Uhuru ni moja ya tunu kubwa za Taifa, ukiwa kichocheo muhimu cha maendeleo, hususan katika kupambana na ujinga, maradhi na umaskini.

Awali, akipokea Mwenge huo, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Chalinze, Ramadhan Possi, alieleza jumla ya miradi saba yenye thamani ya sh. bilioni 34.179 inapitiwa, ambapo miradi mitatu imezinduliwa, mitatu imekaguliwa na mmoja umetembelewa.

Wakati huohuo, Mwang’onda ameridhishwa na utekelezaji wa mradi wa jengo la wagonjwa wa nje (OPD) katika Kituo cha Afya Kiwangwa uliogharimu shilingi milioni 20.583.

Pia Mwenge wa Uhuru umetembelea ujenzi wa boksi kalvati katika barabara ya Mwinyi–Kudiembe, Kata ya Bwilingu, uliotekelezwa kwa gharama ya shilingi milioni 67.3 kupitia TARURA; na kutembelea kiwanda cha Starlinkgulf Trading Co. Ltd (Wallput) kilichojengwa kwa gharama ya zaidi ya sh bilioni 34.

Top News