Na: Dkt. Reubeni Lumbagala, Tanga

Watoto wana haki zao za msingi. Wanapaswa kupendwa, kulindwa, kusikiliza, kupewa malezi na matunzo. Pia, watoto wanapaswa kupewa mahitaji yote ya msingi yaani chakula, mavazi na malazi. Kimsingi, ni wajibu wa msingi kwa wazazi na walezi hukakikisha watoto wanapata haki na mahitaji yao muhimu ili waweze kufurahia maisha kwa kuzingatia kuwa watoto ni kiungo muhimu katika familia na maendeleo ya Taifa.

Serikali kama mdau muhimu wa ustawi na maendeleo ya watoto, inawajibika kuweka mazingira mazuri ya ustawi wa watoto. Aidha, serikali inawajibika kutunga sheria zitakazowalinda watoto ili kesho zao ziweze kutimia na Taifa linufaike kupitia uwepo wao. Ipo changamoto katika jamii zetu kwa baadhi ya wanawake kutupa watoto pindi wanapojifungua watoto hao. 

Wengine huwatupa katika mazingira ambayo ni rahisi kuokotwa na wapita njia lakini baadhi yao huwatupa katika mazingira mabaya mathalani jalalani ambapo kwa bahati mbaya wengine huokotwa wakiwa tayari wameshapoteza maisha. Mbaya sana.

Kwa sababu yeyote ile, suala la kutupa mtoto si suala zuri hasa mtoto anapotupwa katika mazingira mabaya ambayo yanazalisha matatizo mengine mathalani magonjwa kutokana na kupigwa baridi kali na wengine kupoteza maisha kabisa.

 Zipo sababu kadhaa zikiwemo suala la hali ngumu za maisha au baba mzazi wa mtoto kukataa mimba au kumlea mtoto, na hivyo mwanamke kuamua kumtupa mtoto wake aliyehangaika nae kwa miezi tisa tumboni na uchungu wa kumzaa hospitalini.

Januari 17, 2026, karibu na nyumba ya wageni (Guest House) ijulikanayo kwa jina la Kasulu, Nzega Mjini mkoani Tabora, alitelekezwa mtoto ambapo Ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Nzega chini ya uongozi wa Mkuu wa wilaya hiyo, Naitapwaki Tukai pamoja na Jeshi la Polisi wilaya ya Nzega waliamua kumchukua mtoto huyo na kumpeleka hospitali kwa uchunguzi na uangalizi huku jitihada za kumpata mama mzazi wa mtoto huyo zikiendelea.

Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa upendo mkubwa alionao kwa watoto na jamii, ameamua kumchukua mtoto huyo ambaye amepewa jina la Grace Samia Suluhu Hassan. Tukio hilo la upendo limefanyika Machi 11, 2026, katika makazi yake ya Ikulu ya Chamwino Jijini Dodoma. Kipekee kabisa, nimpongeze Rais Dk. Samia kwa moyo wake wa upendo kwa mtoto huyo kwa kuamua kuchukua jukumu la kumuasili awe ni sehemu ya watoto na familia yake kimalezi na kimatunzo.

Rais Dk. Samia anatoa matumaini mapya juu ya hatma ya mtoto huyo kuwa yupo kwenye mikono salama na Mwenyezi Mungu amjalie mtoto huyo afya njema ili akue vizuri. "Wanaotupa watoto hawajui wanalolifanya. Kuliko kumtupa mtoto ni afadhali ukamkabidhi katika mamlaka za kisheria au kituo cha kulelea watoto. Kila mtoto aliyezaliwa ni hazina na hatujui kesho yake," amesisitiza Rais Dk . Samia.

Pengine ni muda muafaka kwa wanaume kutimiza majukumu ya kimalezi badala ya kutelekeza familia, na hivyo kuwaachia wanawake njia panda, hali inayosababisha baadhi ya wanawake kufikia hatua ya kuwatupa watoto. 

Lakini jambo la muhimu ambalo Rais Dk. Samia amelisisitiza ni kutumia vituo vya watoto kuomba msaada ya kulelewa mtoto badala ya kumtupa mtoto, jambo ambalo si zuri hata mbele za Mungu na hata katika maadili yetu ya Kitanzania. Kwa hakika, Rais Dk. Samia ameonyesha upendo wa kipekee kwa jamii kwa kumuasili mtoto Grace Samia Suluhu Hassan. Tumuombee mtoto Grace Samia Suluhu Hassan awe na afya njema na siku moja aje kuwa nguzo muhimu kwa nchi yetu ya Tanzania.

Dk. Reubeni Lumbagala ni Mwalimu katika Shule ya Sekondari Funguni ya wilayani Pangani mkoani Tanga.

Maoni : 0620 800 462.







Na MWANDISHI WETU

ZAIDI ya washiriki 600 kutoka ndani na nje ya nchi wanataraji kushiriki semina maalumu ya uendeleaji na upangaji wa miji inayo kua.

Semina hiyo ya siku mbili imeandaliwa na Chama cha Wabunifu Majengo Tanzania (AAT) itafanyika mjini Morogoro kuanzia Aprili 9-10 mwaka huu.

Akizungumza na waandishi wa habari, jijini Dar es Salaam, Rais wa AAT, Meck T’chawi, amesea ni semina muhimu kwani inagusa kwa kiasi kikubwa suala la upangaji miji na ujenzi wa nyumba bora zinazo zingatia teknolojia ya sasa na zamani.

Ameeleza, teknolojia ya ujenzi inakua kwa kasi hivyo kuleta mabadiliko ya ukuaji wa miji.

“Semina hii itasaidia kutoa elimu ya namna ya kupanga miji inayobadilika kuringana na teknolojia ya sasa na ya zamani,”ameeleza T’chawi.

Amebainisha kwa hapa Tanzania miji mingi ilipangwa enzi za ukoloni kipindi cha Mjerumani ingawa changamoto ni kutokana na ongezeko la idadi ya watu linalofanya miji hiyo kuonekana kama skwata.

“Tunahitajika kufanya mbinu mbanndala ili sasa maeneo yanayoonekana ni skwata kuyapanga. Tunaweza kuomba wafadhili li kutusaidia kupanga maeneo hayo. Tukitumia wataalamu wetu inawezekana,”amesema.

Katibu Mtendaji wa AAT, Attie Ahmed Ali, ametoa wito kwa wataalamu wote kushiriki semina hiyo muhimu kwani inawapa wigo mkubwa kutumia ukuaji wa teknolojia na taaluma zao.

“Katika kuunga mkono jitihada za Raisa Dk. Samia Suluhu Hassan katika kukuza sekta ya utalii, semina hii pia itakuwa na tukio la washiriki kwenda kutalii katika mbuga ya wanyama ya Mikumi iliyopo Morogoro,”amesema Attie.

Mwenyekiti wa maandalizi wa semina hiyo, Fortunata Msakamali, alisema washiriki watatoka katika nchi za Afrika Mashariki, Bara la Afrika na dunia kwa ujumla.

“Itashirikisha wabunifu majengo ndani na nje ya jengo, watu wa mandhari, watu wa teknolojia, wasimamizi wa ujenzi, wasimamizi miradi, mipango miji, wahandisi, wakandarasi, waendelezaji majengo, wahadhili na mafundi,”amebainisha.

Mjumbe wa kamati hiyo Catheline Joseph, alisema wakadiriaji wa majenzi wananafasi kubwa kuhakikisha gharama zinazotokana na mabadiliko ya miji zinakuwa sahihi kwaajili ya miji salama ya vizazi vilivyopo na vya baadaye.







Na Said Mwishehe,Michuzi TV-Njombe

WAKALA wa Nishati Vijijini (REA) umetoa rai kwa sekta binafsi nchini kuchangamkia fursa ya kuwekeza katika miradi midogo ya kuzalisha umeme vijijini kwani wakala huo upo tayari kushirikiana nao kwa kila hatua.

Rai hiyo imetolewa leo Machi 11,2026 na Kaimu Meneja Usaidizi wa Kiufundi kwa Waendelezaji wa Miradi kutoka REA, Mhandisi Emmanuel Yessaya mbele ya Wahariri wa vyombo vya habari ambao ni Wanachama wa Jukwaa la Wahariri Tanzania(TEF)walioko katika ziara ya kutembelea miradi inayosimamiwa au kufadhiliwa na wakala huo mkoani Njombe.

Wahariri hao wamepata nafasi ya kuona mradi wa kuzalisha umeme wa kilovati 317 uliopo kwenye Kijiji cha Boimanda katika kata ya Matola wilayani Njombe mkoani Njombe ambapo REA wametoa ruzuku ya Sh.bilioni 5.4 kujenga miundombinu ya mradi huo unaosimamiwa na Shirika la Benedictine Sisters of St. Gertrud Convent

“Miradi ya uzalishaji umeme inayotekelezwa na sekta binafsi ina mchango mkubwa katika kuongeza upatikanaji wa nishati ya uhakika nchini.Hivyo tunaendelea kutoa rai kwa sector binafsi kushiriki katika miradi ya aina hii hasa katika mikoa kama Iringa,Njombe na Ruvuma ambako kuna vyanzo vya maji vinavyoweza kutumika kuzalisha umeme.”

Kuhusu mradi huo wa umeme wa maji Mhandisi Yessaya amesema hadi sasa ujenzi wa miundombinu ya mradi huo umekamilika na kilichobaki ni kuwasha mtambo na kuunganisha umeme katika gridi ya taifa.

Amefafanua kuwa “Mradi huu ulianzishwa kuzalisha umeme kwa matumizi ya shirika ambalo linashughuli mbalimbali zinazohitaji umeme ikiwemo katika hospitali, shule, karakana na gereji.Baadae ulipanuliwa ili kunufaisha jamii kwa kuunganisha vijiji vitatu vya Matola, Boimanda na Kitulila.Hata hivyo REA tulishapeleka umeme katika Vijiji vyote vya Mkoa wa Njombe.”

Wakati huo huo Mratibu wa Mradi wa kuzalisha umeme wa Lupali, Sister Imaculatha Mlowe, amesema REA imechangia kwa kiasi kikubwa kufanikisha kukamilika kwa mradi huo kwani amekuwa Mdau muhimu tangu hatua za awali.

Pia amesema kwa hivi sasa zaidi ya wananchi 212 wa Kijiji cha Boimanda wanapata huduma ya umeme wa TANESCO wakati wananchi 366 wa Kijiji cha Matola wanapata umeme kupitia mradi wa zamani wa Lupali.

Aidha amesema mkataba wa kuuza umeme kati ya TANESCO na Shirika la St. Benedictine of Imiliwaha tayari umeshasainiwa na kazi ya kuanza uzalishaji zinatarajiwa kukamilika ndani ya miezi mitatu ijayo.







 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amewasihi Viongozi wa dini na Watanzania kwa ujumla kutumia mwezi wa toba wa Ramadhani na Kwaresma kuiombea Nchi, Viongozi wa Serikali na Vyama vya Siasa ili kujenga nchi moja yenye upendo na mshikamano.

Makamu wa Rais, amesema hayo mara baada ya kushiriki Iftari aliyoiandaa kwaajili ya wananchi mbalimbali wa Mkoa wa Dodoma pamoja na Viongozi wa Serikali, Taasisi za Dini na Chama Cha Mapinduzi, iliyofanyika Mkoani Dodoma.

Amesema jambo kubwa ni kuhakikisha hamasa ya mapenzi ya nchi inakuwepo kwa kila mmoja na chemchem ya mapenzi kwa nchi iwepo katika roho ya kila mtanzania ili kuishi kwa kupendana na kushirikiana chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

 Pia, Makamu wa Rais amesema katika mambo ya maana yanayoweza kufanyakika katika mwezi wa toba ni pamoja na kumuahidi Mwenyezi Mungu kwamba kila mtanzania atafanya jitihada ya kuunganisha watanzania kujenga nchi kuwa nchi moja yenye upendo.

Iftar hiyo imehudhuriwa na Viongozi mbalimbali akiwemo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhandishi Hamad Masauni, Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro, Waziri wa Madini Anthony Mavunde, Kamati ya Maridhiano, Viongozi mbalimbali wa Dini, Wabunge wa Mkoa wa Dodoma, Wakuu wa Wilaya pamoja na wananchi.

















-Asisitiza Ushirikiano wa Kimataifa, Majadiliano ya Kimkakati na mbinu za pamoja kukabiliana na changamoto za kidunia.

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Stephen Mbundi amekutana na Washiriki wa Kozi ya 14 kutoka Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC) waliotembelea Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mtumba jijini Dodoma kwa ziara ya Mafunzo.

Akizungumza katika kikao na wanachuo hao Mhe. Balozi Mbundi alieleza kufurahishwa kwake na ziara hiyo ambayo inawapatia mafunzo kwa vitendo wanachuo hao na kusisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa, majadiliano ya kimkakati, na mbinu za pamoja kama nyenzo za kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazoikabili dunia.

Alisema kuwa mazingira ya usalama duniani yanabadilika kutokana na changamoto mbalimbali kama za mivutano ya kisiasa kati ya mataifa, uhalifu wa kuvuka mipaka, ugaidi, vitisho vya mtandao, mabadiliko ya tabianchi na za kiuchumi.

Aliongeza kuwa ni matumaini yake ziara hiyo itachangia kuimarisha uelewa wa washiriki kuhusu uhusiano kati ya diplomasia, usalama wa taifa na ushirikiano wa kimataifa na kuimarisha ushirikiano kati ya Wizara ya Mambop ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Chuo hicho.

Katika kikao hicho Balozi Mbundi alielezea kwa ufupi historia, majukumu, dira na dhamira ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki katika kusimamia sera ya mambo ya nje, kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia, na kukuza ushirikiano wa kikanda kupitia taasisi kama Jumuiya ya Afrika Mashariki na Umoja wa Afrika.

Naye Mwakilishi wa Mkuu wa Chuo cha NDC, Brigedia Jenerali Selemani Bakari Gwaya alieleza kuridhishwa kwao na mchango wa Wizara katika kufanikisha kozi mbalimbali zinazotolewa na chuo hicho ambao unakiwezesha kukua kimataifa na kuaminika kama taasisi ya kimkakati.

Amepongeza juhudi za Wizara kwa kuendelea kutekeleza diplomasia ya uchumi kwa weledi na Vitendo licha ya changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika siasa za kimataifa.

Wanachuo 72 wa Kozi ya 14 ya NDC kutoka nchi 17 za Tanzania, Bangladesh, Botswana, Burundi, Misri, Ethiopia,India, Kenya, Malawi, Namibia, Nigeria, Rwanda, Sierra Leone, Afrika Kusini, Uganda, Zambia na Zimbawe waliambatana na Wakufunzi na Viongozi wao walifika Wizarani kwa lengo la kujifunza jinsi Wizara inavyotekeleza majukumu yake.












Na Mwandishi Wetu, Songea na Iringa

Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imewakutanisha wazabuni na Taasisi Nunuzi wa mikoa ya Ruvuma, Iringa na Njombe na kuwajengea uwezo kuhusu Moduli ya kupokea na kushughulikia Malalamiko na rufaa kwenye mfumo wa NeST kwa lengo la kuimarisha utendaji kazi. 

Mafunzo hayo yamefanyika kwa nyakati tofauti katika miji ya Songea na Iringa yamewahusisha washiriki 380 ambao ni wazabuni, wataalamu wa ununuzi, sheria, Tehama pamoja na makundi maalum yakiwemo wanawake, vijana, wazee na watu wenye mahitaji maalum pamoja na mafundi wa ndani.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando amesema mafunzo hayo yamekuwa yakitolewa na PPAA kwa kushirikiana na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) kwa lengo la kuwajengea uwezo wazabuni na Taasisi Nunuzi ili kuwapa ufanisi zaidi wakati wa utekelezaji wa majukumu yao, hususan katika kushughulikia malalamiko na migogoro itokanayo katika michakato ya ununuzi wa Umma. 

“Mafunzo haya yanalenga kuimarisha utendaji kazi wenu, kuhakikisha ufanisi, kuongeza uelewa wa matumizi ya Moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika wa Mfumo wa Ununuzi wa Umma kwa Njia ya Kielektroniki (NeST),” amesema Bw. Sando 

Bw. Sando ameongeza kuwa, katika kutimiza azma ya Serikali mafunzo yamewashirikisha vijana, wanawake na makundi maalum katika ununuzi wa umma ili kuwawezesha kupata elimu kuhusu ununuzi wa Umma hususan katika michakato ya ununuzi na kuhakikisha kuwa wanaisaidia Serikali kupata thamani halisi ya fedha katika miradi ya kimkakati yenye tija kwa Taifa.  

Pamoja na mambo mengine, Bw. Sando amewasihi washiriki kutumia mafunzo hayo kujifunza namna moduli ya kuwasilisha malalamiko na rufaa inavyofanya kazi katika Mfumo wa NeST kwani inatoa njia rahisi, ya haraka na yenye uwazi kwa wadau wote kushiriki katika mchakato wa ushughulikiaji wa malalamiko yanayotokana na michakato ya zabuni za umma. 

“Matumizi ya moduli yameongeza ufanisi katika usimamizi wa rufaa, kupunguza muda wa kushughulikia mashauri, na kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika utoaji wa haki, kuokoa muda na kupunguza gharama zinazohusiana na usuluhishi wa migogoro ya ununuzi,” ameongeza Bw. Sando

Kwa upande wake Meneja wa Usimamizi wa Rufaa na Sheria (PPAA), Bi. Florida Mapunda amesema kuwa mafunzo hayo yamelenga kutoa elimu kwa wadau wa ununuzi wa Umma kuhusu taratibu za uwasilishaji na ushughulikiaji wa malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST. 

“PPAA kwa kushirikiana na PPRA tumejenga moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko katika mfumo wa NeST ili kuwasaidia wadau wa ununuzi wa umma (Wazabuni na Taasisi za Umma) kuwasilisha malalamiko na rufaa kwa ufanisi zaidi kupitia mtandao,” amesema Bi. Mapunda.Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando akifungua mafunzo kuhusu Moduli ya kupokea na kushughulikia Malalamiko na rufaa kwenye mfumo wa NeST kwa wazabuni na Taasisi Nunuzi wa Mkoa wa Ruvuma. Kushoto ni Meneja wa Usimamizi wa Rufaa na Sheria (PPAA), Bi. Florida Mapunda na kulia ni Mkuu wa Sehemu ya Sheria PPAA, Bi. Agnes Sayi. Meneja wa Usimamizi wa Rufaa na Sheria (PPAA), Bi. Florida Mapunda akiwasilisha mada kuhusu uwasilishaji na ushughulikiaji wa malalamiko katika mfumo wa NeST kwa wazabuni na Taasisi Nunuzi walioshiriki mafunzo mkoani Ruvuma.
 Afisa Sheria kutoka PPAA, Bw. Venance Mkonongo akiwasilisha mada kuhusu uwasilishaji na ushughulikiaji wa malalamiko na rufaa katika ununuzi wa umma kwa wazabuni na Taasisi Nunuzi walioshiriki mafunzo mkoani Ruvuma.
Mkuu wa Sehemu ya Sheria PPAA, Bi. Agnes Sayi akiwasilisha mada kwa washiriki walioshiriki mafunzo kuhusu Moduli ya kupokea na kushughulikia Malalamiko na rufaa kwenye mfumo wa NeST kwa wazabuni na Taasisi Nunuzi wa Mikoa ya Iringa na Njombe. 
Mwezeshaji kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Bw. Daniel Kimaro akiwasilisha kuhusu utoaji wa tuzo, uandaaji, upekuzi, na utiaji saini wa mkataba kwa wazabuni na Taasisi Nunuzi wa Mikoa ya Iringa na Njombe. Sehemu ya wazabuni na Taasisi Nunuzi walioshiriki mafunzo kutoka Mikoa ya Iringa na Njombe

Viongozi wa PPAA wakiongozwa na Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando, katika picha ya pamoja na Kundi la wazabuni wenye mahiotaji maalum. Wengine pichani ni Meneja wa Usimamizi wa Rufaa na Sheria (PPAA), Bi. Florida Mapunda (kushoto)na kulia ni Mkuu wa Sehemu ya Sheria PPAA, Bi. Agnes Sayi.

 


Top News