Tanzania imepiga hatua katika kuelekea kujitosheleza kwa sukari kufuatia kuanza rasmi kwa uzalishaji katika Kiwanda kipya cha Kisasa cha Sukari Kilombero K4 kilichopo mkoani Morogoro, ambacho kimegharimu zaidi ya shilingi bilioni 700.
Uwekezaji huo unatarajiwa kuongeza uzalishaji wa sukari nchini, kupunguza utegemezi wa uagizaji kutoka nje na kuchochea ukuaji wa uchumi.
Akizungumza katika maonesho ya nanenane Kanda ya Mashariki Mkurugenzi wa Biashara wa Kiwanda cha Sukari Kilombero, Fimbo Butallah, amesema kuanza kwa uzalishaji katika kiwanda hicho kutasaidia kuziba pengo la upungufu wa sukari nchini na kuongeza upatikanaji wa bidhaa hiyo kwa wananchi.
Butallah amesema pia kiwanda hicho kimezingatia tofauti za vipato vya Watanzania kwa kuzalisha sukari katika ujazo wa aina mbalimbali, hatua itakayowezesha wananchi kupata bidhaa hiyo kulingana na uwezo wao wa kifedha.
Kwa upande wake, Meneja wa Ufuatiliaji na Uthibitishaji kutoka Bodi ya Sukari Tanzania, Bahati Hakimu, amesema kukamilika kwa Kiwanda cha Kilombero K4 ni hatua muhimu katika kuongeza uzalishaji wa sukari nchini, huku pia kikitarajiwa kuongeza ajira kwa wakulima wa miwa na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika Bonde la Kilombero.
Na Janeth Raphael -MichuziTv
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametoa wito kwa viongozi wa nchi za Afrika kuharakisha utekelezaji wa miradi ya miundombinu, akisisitiza kuwa maendeleo ya Bara hilo hayatapimwa kwa mipango na sera pekee, bali kwa matokeo yanayoonekana katika maisha ya wananchi.
Rais Samia ameyasema hayo leo jijini Dar es Salaam wakati akifungua Jukwaa la Miundombinu Afrika pamoja na Mkutano Mkuu wa Wanahisa wa Africa50, ambapo alieleza kuwa uwekezaji katika miundombinu ni nguzo muhimu ya kukuza uchumi, kuongeza ushindani wa Afrika, kuvutia wawekezaji na kuimarisha biashara ndani ya bara.
Amesema wananchi wanahitaji kuona matokeo kupitia ujenzi wa barabara bora, reli za kisasa, bandari zenye ufanisi, nishati ya uhakika, maendeleo ya teknolojia pamoja na kuongezeka kwa fursa za ajira.
Akizungumzia hatua zinazochukuliwa na Tanzania, Rais Samia alisema Serikali inaendelea kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kujenga uchumi wa viwanda, jumuishi na unaotegemea ubunifu, ujuzi pamoja na miundombinu ya kisasa.
Amebainisha kuwa Serikali imeendelea kuwekeza katika kuboresha Bandari ya Dar es Salaam, Reli ya Kisasa (SGR), barabara, madaraja na korido za kimkakati ili kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha biashara na usafirishaji katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika.
Rais Samia amesema uwekezaji huo hauwanufaishi Watanzania pekee, bali pia unahudumia nchi jirani zisizo na bandari, zikiwemo Burundi, Rwanda, Uganda, Zambia, Malawi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), hivyo kuimarisha nafasi ya Tanzania kama lango muhimu la biashara na uwekezaji barani Afrika.
Aidha, amesisitiza kuwa Afrika inapaswa kuongeza thamani ya rasilimali zake badala ya kuendelea kusafirisha malighafi, hatua ambayo itaongeza ajira, ujuzi na uwezo wa uzalishaji ndani ya bara.
Katika sekta ya nishati, Rais Samia alieleza kuwa gesi asilia ina nafasi kubwa katika kuimarisha usalama wa nishati, kusaidia ukuaji wa viwanda na kuchochea maendeleo ya uchumi wa Tanzania pamoja na nchi nyingine za Afrika.
Kwa upande wake, Naibu Rais wa Kenya, Prof. Kithure Kindiki, alisema mafanikio ya miradi mikubwa ya miundombinu yanategemea uongozi madhubuti wa kisiasa, sera thabiti na mipango ya muda mrefu.
Prof. Kindiki pia amezitaka nchi za Afrika kuwekeza katika kujenga uwezo wa wataalamu wa ndani, kutumia mifumo bunifu ya kugharamia miradi na kuhakikisha wananchi wanashirikishwa kikamilifu ili wanufaike na maendeleo yanayotekelezwa.
Naye Mwenyekiti wa Africa50 ambaye pia ni Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Dkt. Sidi Ould Tah, alisema taasisi hiyo itaendelea kusaidia nchi za Afrika kubadilisha fursa za miundombinu kuwa miradi inayoweza kufadhiliwa na kutekelezwa kwa ufanisi.
Amesema katika muongo wa pili wa Africa50, kipaumbele kitakuwa kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi, kuhamasisha mitaji na kuimarisha ushirikiano kati ya serikali, taasisi za fedha na sekta binafsi.
Mkutano huo pia ulihusisha mjadala wa mawaziri kutoka Tanzania, Msumbiji, Nigeria na Senegal kuhusu matumizi ya gesi asilia, maendeleo ya viwanda, kuongeza thamani ya rasilimali na ujenzi wa miundombinu ya kikanda.
Katika mjadala huo ilielezwa kuwa zaidi ya Waafrika milioni 600 bado hawana huduma ya umeme, huku Tanzania ikitajwa kuongeza upatikanaji wa nishati safi ya kupikia kutoka asilimia sita mwaka 2021 hadi asilimia 28 mwaka 2026.
Sambamba na mkutano huo, Tanzania ilisaini makubaliano mbalimbali ya ushirikiano yanayolenga kupanua huduma za matibabu ya figo, kuendeleza miradi ya usafirishaji wa umeme kwa ubia wa sekta ya umma na binafsi, pamoja na kuongeza matumizi ya gesi asilia katika shughuli za viwanda.
Makubaliano hayo yanahusisha Africa50, Wizara ya Afya, Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) pamoja na kampuni ya TAQA Arabia.
Akihitimisha hotuba yake, Rais Samia aliipongeza Africa50 kwa mchango wake katika kuendeleza ajenda ya miundombinu barani Afrika na kusisitiza kuwa makubaliano yote yaliyofikiwa yanapaswa kutekelezwa kwa haraka ili yaweze kuleta manufaa ya moja kwa moja kwa wananchi.



Na OWM – TAMISEMI, Morogoro
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amewapongeza wakulima, wafugaji na wavuvi kwa mchango wao mkubwa uliowezesha Tanzania kufikia utoshelevu wa chakula wa zaidi ya asilimia 120, hatua inayodhihirisha mafanikio ya uwekezaji unaoendelea kufanywa na Serikali katika sekta za kilimo, mifugo na uvuvi.
Dkt. Mwigulu aliwasilisha pongezi hizo za Mhe. Rais Agosti 4, 2026, alipotembelea Maonesho ya Nane Nane Kanda ya Mashariki yanayofanyika katika Viwanja vya Nane Nane mkoani Morogoro.
Katika ziara hiyo alijionea shughuli na ubunifu wa wakulima, wafugaji na wavuvi kutoka mikoa ya Morogoro, Dar es Salaam, Pwani na Tanga.
Amesema maonesho ya mwaka huu yanaongozwa na kaulimbiu isemayo, "Tambua Soko; Ongeza Tija Kutekeleza Dira 2050," ambayo inawahimiza Watanzania kuzalisha kwa kuzingatia mahitaji ya soko, kutumia teknolojia za kisasa, kuongeza ubora wa bidhaa na kuimarisha mnyororo wa thamani ili kufanya kilimo kuwa biashara yenye tija na mchango mkubwa katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
"Kwa nilichojionea kupitia maonesho ya mwaka huu, ninaziona dalili zote kwamba ifikapo mwaka 2050 malengo ya Dira ya Taifa tuliyojiwekea yatakuwa yamefikiwa, kwa kuwa tuko kwenye hatua nzuri ya utekelezaji katika sekta za kilimo, mifugo na uvuvi," amesema Dkt. Mwigulu.
Ameongeza kuwa ameridhishwa na ubora wa mazao mbalimbali yaliyooneshwa, ikiwemo nyanya, bilinganya na bidhaa nyingine zinazokidhi viwango vya masoko ya kimataifa, yakiwemo ya Marekani na Ulaya, jambo linaloashiria kuwa Tanzania ipo kwenye mwelekeo sahihi wa kuzalisha bidhaa zenye ushindani duniani.
Akizungumzia sekta ya mifugo na uvuvi, Dkt. Mwigulu amesema zimeendelea kuwa nguzo muhimu za uchumi wa taifa, akibainisha kuwa mchango wa sekta ya mifugo katika pato la taifa umeongezeka kutoka asilimia 2.3 hadi asilimia 6.2.
Ametoa mfano wa mafanikio ya wanaonufaika na sekta hiyo kwa kumtaja kijana mmoja mhitimu anayejihusisha na ufugaji wa kisasa, ambaye ameonesha ng'ombe mwenye uzito wa zaidi ya kilogramu 1,000 mwenye thamani ya takribani Shilingi Milioni 20. Aidha, amesema kijana huyo anafuga zaidi ya ng'ombe 200 na alipoulizwa na Waziri wa TAMISEMI kama anahitaji mkopo, alieleza kuwa hana uhitaji huo kutokana na mafanikio ya shughuli zake.
Awali, akitoa neno la utangulizi kabla ya Waziri Mkuu kuzungumza na wananchi pamoja na washiriki wa maonesho hayo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, alisema Waziri Mkuu alimpa jukumu la ulezi wa Mkoa wa Morogoro, hivyo alimkaribisha rasmi kama waziri mwenyeji wa mkoa huo, ambao ni mmoja wa mikoa inayounda Kanda ya Mashariki katika Maonesho ya Nane Nane.
Jumla ya taasisi za umma 54 zinatarajiwa kuwasilisha taarifa za utendaji wa uwekezaji mbele ya Kamati za Kudumu za Bunge kwa muda wa wiki tatu, katika mchakato unaolenga kuwezesha uchambuzi wa thamani na utendaji wa mitaji ya umma pamoja na utekelezaji wa mipango ya kimkakati ya taasisi husika.
Katika awamu hii iliyoanza Jumatatu, Agosti 3, 2026, taasisi hizo zimepangwa kuwasilisha taarifa zao mbele ya Kamati mbili za Kudumu za Bunge, ambapo 27 zitawasilisha mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) na nyingine 27 mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Umma (PAC).
Hadi Jumatano, Agosti 5, 2026, taasisi nne zilikuwa tayari zimewasilisha taarifa zao mbele ya Kamati.
Taasisi hizo ni Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL), Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB), Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA) na Wakala wa Huduma za Ununuzi Serikalini (GPSA), huku Kamati zikionesha kuridhishwa na utendaji wa taasisi husika.
Uwasilishaji huo ni sehemu ya utekelezaji wa jukumu la kusimamia na kufuatilia utendaji wa uwekezaji wa Serikali kupitia taasisi na kampuni zilizo chini ya usimamizi wa Ofisi ya Msajili wa Hazina (OTR).
OTR inasimamia taasisi na kampuni 308, zikiwemo taasisi za umma 252 na kampuni 56 ambazo Serikali ina umiliki wa hisa chache, huku jumla ya uwekezaji katika taasisi na kampuni hizo ikiwa Sh92.3 trilioni.
Kaimu Msajili wa Hazina, Bi Lightness Mauki, alisema uwasilishaji huo unaipa Bunge fursa ya kupata picha ya kina kuhusu mwenendo wa uwekezaji wa mitaji ya umma.
“Uwasilishaji wa taarifa hizi ni moja ya utaratibu wa Bunge katika kusimamia Serikali, ikiwemo usimamizi wa uwekezaji wa mitaji ya umma,” alisema Bi. Mauki, ambaye pia ni Mkurugenzi wa Usimamizi wa Utendaji wa Mashirika ya Kibiashara.
Taarifa hizo huwezesha kuangalia thamani ya mitaji, mapato na matumizi, faida, hali ya mizania pamoja na utekelezaji wa mipango ya kimkakati ya taasisi husika, ikiwa ni msingi wa uwajibikaji na utawala bora,” alisema Mauki.
Uwasilishaji wa taarifa hizo unafanyika kwa mujibu wa Kanuni ya 11 ya Kanuni za Kudumu za Bunge, inayozipa Kamati jukumu la kuchambua na kubaini iwapo utekelezaji wa miradi ya uwekezaji wa umma unafanyika kwa ufanisi na kwa kuzingatia taratibu, sheria na miongozo ya biashara.
Kwa mujibu wa Bi. Mauki, Kamati pia inachambua na kujadili taarifa zinazohusu uwekezaji katika mashirika ya umma na kampuni ambazo Serikali inamiliki hisa.
Alisema OTR inaratibu mchakato huo na kuhakikisha taarifa zinazowasilishwa zinaakisi kwa usahihi na uwazi hali halisi ya utendaji wa taasisi na mashirika ya umma, ili kuwezesha Kamati za Bunge kufanya uchambuzi na kutoa ushauri na maelekezo yanayolenga kuimarisha utendaji.
“Jukumu la Ofisi ya Msajili wa Hazina katika zoezi hili ni kuratibu na kuhakikisha taarifa za mashirika ya umma zinakuwa na ukweli na uwazi wa hali halisi wa utendaji wa taasisi hizo ili kutoa fursa kwa Kamati za Bunge kushauri na kuelekeza katika masuala mbalimbali yanayolenga kuimarisha utendaji wa mashirika ya umma,” alifafanua Mauki.
Uwasilishaji wa taarifa za mashirika hayo ulitanguliwa na uwasilishaji wa Taarifa kuhusu hali ya Uwekezaji wa Umma hadi kufikia Mwaka 2024/2025 mbele ya PIC.
Taarifa hiyo, iliyowasilishwa na Bi. Mauki, ilijikita katika kuonesha hali ya uwekezaji wa Serikali ndani na nje ya nchi, mgawanyo wa uwekezaji katika mashirika ya umma, mapato yasiyo ya kodi ya mashirika na taasisi za umma, mikopo ya mashirika na taasisi za umma pamoja na taarifa za dhamana na misaada katika mashirika hayo.
Mchakato huo unaendelea kutoa fursa kwa Bunge kuchambua mwenendo wa uwekezaji wa mitaji ya umma na kutoa maoni na maelekezo yanayoweza kusaidia kuimarisha utendaji, uwajibikaji na matumizi yenye tija ya rasilimali za umma.
Elimu hiyo iliyotolewa katika ofisi za Ngorongoro ilijumuisha wadau muhimu wanaoguswa na mpango huo ambao ni viongozi wa jamii, wanafunzi pamoja na wadau mbalimbali ambao wamepewa uelewa kuhusu vigezo vya mkopo, sifa za waombaji pamoja na kupitia na kujadili mwongozo wa programu ya Ngorongoro Scholarship Fund.
Katika kikao hicho, viongozi wa jamii wamepongeza hatua ya Mamlaka ya kushirikiana na HESLB katika kuandaa na kuboresha mwongozo wa mfuko huo, wakieleza kuwa utasaidia kuweka utaratibu unaozingatia usawa, uwazi na mahitaji ya wakati katika kuwawezesha wanafunzi wenyeji kupata fursa za elimu ya juu.
Mwenyekiti wa Baraza la Wafugaji Ngorongoro, Mhe. Edward Maura, aliipongeza Mamlaka ya Ngorongoro na HESLB kwa kutoa elimu kuhusu Ngorongoro Scholarship Fund hasa jinsi wanufaika wanavyoweza kutambua fursa, kujaza fomu na kufuata taratibu za kuomba ufadhili.
“Tunawapongeza Ngorongoro na Bodi ya Mikopo kwa kutoa elimu hii kwa jamii na wanafunzi na kusaidia kuwaondolea wanafunzi changamoto na uelewa mdogo wa namna ya kuomba na kupata mikopo huu, tunaamini maamuzi haya ya Serikali yanalenga kuimarisha mahusiano kati ya jamii na Ngorongoro na tunaamini wanafunzi na jamii watatumia fursa zinazotolewa kwa kuzingatia taratibu zilizowekwa” alisema Mh. Maura.
Utekelezaji wa program hii unalenga kuimarisha ushirikiano na kuboresha huduma za jamii kwa wananchi wa Ngorongoro ambapo elimu wanayopata itasaidia ushiriki wao katika program za uhifadhi endelevu na kuvutia wageni kupitia vivutio vya utalii vilivyopo.






.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)















.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)




.jpeg)





.jpeg)




