Na Lusungu Helela, Dodoma 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhwani Kikwete, amesema uamuzi wa Serikali ya Somalia kumtuma Waziri mwenye dhamana ya Utumishi wa Umma nchini Tanzania ni ishara ya kutambua mafanikio yaliyofikiwa na Tanzania katika eneo la matumizi ya mifumo katika masuala ya Utumishi wa Umma nchini. 

Mhe. Kikwete amesema hayo leo jijini Dodoma wakati akizungumza na ujumbe wa Serikali ya Somalia unaoongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Masuala ya Utumishi wa Umma, Hirsi Jama Ganni, uliofika nchini kwa ziara ya kikazi ya siku tatu. 

Amesema ujio wa ujumbe huo unaonyesha kuwa Somalia inatambua na kuthamini uzoefu wa Tanzania katika uendeshaji wa Serikali, utumishi wa umma na matumizi ya mifumo ya kidijitali katika utoaji wa huduma kwa wananchi. 

“Ukiona wenzako wanakufuata hasa katika eneo hili ambalo sisi ni watoa huduma, ni wazi kuwa huduma tunayotoa wapo wenzetu wanatambua na kuthamini tunachokifanya na ndiyo maana wameamua kuja kujifunza na kupata uzoefu,” amesema Mhe. Kikwete 

Amesema anaamini uzoefu ambao Somalia itaupata kupitia ziara hiyo utasaidia kuboresha zaidi masuala ya utumishi wa umma nchini humo. 

Mhe. Kikwete amesema ujumbe huo unapata fursa ya kujifunza maeneo mbalimbali, ikiwemo namna Serikali inavyohusiana na wananchi, uratibu wa masuala ya kazi na ajira, usalama wa wafanyakazi mahali pa kazi pamoja na mifumo ya pensheni kwa watumishi wanaostaafu katika taasisi za Serikali na sekta binafsi. 

“Hii ziara ni kielelezo tosha kuwa Somalia imedhamiria, ndiyo maana haijaweza kutuma maafisa pekee, lakini Waziri mwenye dhamana ya Utumishi wa Umma ameamua kuja mwenyewe na timu yake kwa lengo la kujifunza na kuja kuona kwa macho yake kazi kubwa iliyofanyika Tanzania,” amesisitiza Mhe. Kikwete 

Kwa upande wake, Mhe. Ganni amesema ujumbe wake umefika Tanzania kujifunza namna Tanzania ilivyofanikiwa katika masuala ya utumishi wa umma, hususan matumizi ya mifumo ya kidijitali katika kuboresha utoaji wa huduma. 

Amesema Tanzania imekuwa ikifanya vizuri katika utoaji wa huduma kwa wananchi, huku watumishi wa umma wakitumia mifumo ya kidijitali kuwahudumia wananchi na kuhakikisha wanapata haki zao. 

Mhe. Ganni amesema ujio wao ni muhimu kutokana na hatua ambazo Tanzania imepiga katika kuboresha utendaji wa Serikali na utoaji wa huduma kwa wananchi. 

Amesema wamevutiwa pia na namna mifumo ya Serikali inavyowawezesha watumishi kuwahudumia wananchi kwa ufanisi. 

Akizungumzia mfumo wa e-Mrejesho, Mhe.Ganni amesema ni miongoni mwa mifumo waliyoona ina umuhimu katika kuimarisha mawasiliano kati ya Serikali na wananchi, hivyo wanatarajia kujifunza namna unavyofanya kazi na uwezekano wa kutumia uzoefu huo katika kuboresha huduma nchini Somalia. 

Ziara hiyo ya ujumbe wa Somalia inalenga pia kujifunza kuhusu mifumo ya Baraza la Mawaziri, usimamizi wa rasilimali watu, uajiri kwa kuzingatia sifa, Serikali mtandao, usimamizi wa ajira na mifumo ya taarifa za soko la ajira. 

Ujumbe huo pia unatarajiwa kutembelea Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano pamoja na Mji wa  Serikali Mtumba jijini Dodoma, kwa ajili ya kujionea namna shughuli za Serikali zinavyoratibiwa na kutekelezwa.














 

Na OWM (KAM) Dar es Salaam

Serikali imesema itaendelea kuhakikisha vijana nchini wanaendelea kunufaika na fursa za nje ya nchi na zenye staha kwa kushirikiana na wadau wa ndani na nje ya nchi.

Akizungumza jijini Dar es Salaam Agosti 27,2026 wakati wa uzinduzi wa mkopo wa Ughaibuni Loan unaoratibiwa na Benki ya CRDB pamoja na kuwaaga vijana 130 kati ya 530 wanaotarajia kwenda kufanya kazi nje ya nchi, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Dkt. Evaline Munisi amesema Serikali inatambua ajira za nje ya nchi kama nyenzo muhimu ya kupanua fursa za ajira, kuongeza kipato cha vijana, kukuza ujuzi na kuwajengea uzoefu wa kimataifa.

“Matokeo ya jitihada hizi yamewezesha Watanzania 14,613 kupata ajira nje ya nchi tangu Serikali ya Awamu ya Sita kuingia madarakani. Kati ya Julai 2025 hadi sasa, Watanzania 8,428 wameunganishwa na waajiri nje ya nchi,” amesema Dkt. Munisi.

Amesema mafanikio hayo yameifanya Tanzania kuendelea kuaminika kuwa na nguvu kazi salama na yenye staha duniani.

Kuhusu uzinduzi wa Ughaibuni Loan, Dkt. Munisi amesema mkopo huo unalenga kuwawezesha vijana waliopata ajira nje ya nchi kupata fedha nafuu za kugharamia maandalizi ya safari ikiwemo tiketi ya ndege, bima na visa.

“Ughaibuni Loan siyo msaada bali ni mkopo wa uwezeshaji. Nawasihi vijana wahakikishe wanafanya marejesho ili na wengine wapate fursa,” amesisitiza.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa CRDB, Bw. Pendason Philemon amesema benki imetenga jumla ya Shilingi bilioni 250 kwa miaka mitano kutoa mikopo ya kati ya Sh. 500,000 hadi milioni 20 kwa kila kijana kulingana na gharama za kufika kwa mwajiri wake.

“Kigezo muhimu ni kuwa na mkataba au barua ya ajira iliyothibitishwa na wakala. Marejesho yatakuwa kwa miezi 24 na tunatoa kipindi cha neema cha miezi 2 kwa riba ya asilimia 15,” amesema Philemon.

Mwenyekiti wa Chama cha Mawakala Binafsi wa Ajira TRAA, Bw. Abdala Khalid amesema mkopo huo utawaepusha vijana na watu wasio na nia njema.

Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Bi. Zuhura Yunus amesema Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi,Ajira na Mahusiano inaendelea kutafuta masoko ya uhakika ya ajira ikiwemo Saudi Arabia, Oman, Qatar, Denmark na Ujerumani.

Mmoja wa wanufaika, Dickson Tadeo Mbaga amesema kupitia mkopo huo aliweza kugharamia visa, tiketi na bima. “Ninawasihi vijana wenzangu wachangamkie fursa hii,” amesema.

Serikali imesema itaendelea kuhakikisha vijana 530 wanaokwenda kufanya kazi ughaibuni katika fani mbalimbali ikiwemo ujenzi wanalindwa na kazi zao zinakuwa zenye staha.






 

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026, Ndugu Wazo Michael Mwang’onda, leo tarehe 28 Agosti 2026 amezindua rasmi kituo kipya cha Polisi cha Musasa kilichopo Kata ya Runzewe Magharibi, Wilaya ya Bukombe.

Akizungumza wakati wa uzinduzi, Mwang’onda amewapongeza uongozi wa Musasa Gold Mine kwa kugharamia ujenzi wa kituo hicho na kuiomba jamii kuendelea kushirikiana na wawekezaji katika kuleta maendeleo.

Kwa upande wake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Kamishna Msaidizi wa Polisi Safia Jongo, amesema kituo hiki ndicho kitakuwa kikuu kwa Kata yote ya Runzewe. Amesema wananchi wa Musasa na Runzewe kwa ujumla watahudumiwa huduma zote za kipolisi kupitia kituo hicho.

Ujenzi wa kituo hiki ulianza tarehe 16 Machi 2026 na umegharimu *shilingi 150,000,000. Kati ya hizo shilingi 145,000,000 zimetolewa na Musasa Gold Mine huku wananchi wakichangia shilingi 5,000,000 kupitia nguvu zao. Mgodi pia umenunua samani zote za ofisi.

Uanzishwaji wa kituo hiki umetokana na ongezeko la watu katika eneo hilo kutokana na shughuli za uchimbaji madini. Viongozi wamesema uwepo wake utasaidia kuimarisha ulinzi, kupunguza uhalifu, kutoa mwitikio wa haraka na kukuza mazingira salama kwa uwekezaji.

Wananchi wameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita na wawekezaji kwa hatua hiyo na wameahidi kulinda miundombinu hiyo.






WANAFUNZI 34 waliochaguliwa kupitia mpango wa ufadhili wa Samia Scholarship Extended wameondoka nchini leo Agosti 28, 2026 kuelekea Ireland kwa ajili ya kuanza masomo ya shahada katika fani za Sayansi ya Data, Akili Unde na Sayansi Shirikishi, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali kuandaa wataalamu wa sayansi na teknolojia.

Akizungumza wakati wa kuwaaga wanafunzi hao, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Siylvia Lupembe amesema kundi hilo ni sehemu ya wanafunzi 50 waliochaguliwa kwenda kusoma katika vyuo bora duniani, ambapo wanafunzi 16 tayari wamekwenda Afrika Kusini na wanafunzi 34 waliobaki ndo wameondoka leo kwenda Ireland.

Lupembe amesema wanafunzi hao watasoma katika vyuo viwili nchini Ireland, kikiwemo Chuo Kikuu cha Limerick, na kwamba mbali na masomo ya darasani, watapata pia fursa ya kufanya mafunzo kwa vitendo katika kampuni kubwa za teknolojia.

"Leo hawa ambao tunawaaga hapa uwanja wa ndege ni 34. Wanaenda Ireland na watasoma katika vyuo viwili, masomo hayo hayo ya Sayansi ya Data, Akili Unde na Sayansi Shirikishi, pamoja na mafunzo mengine yanayohusiana na teknolojia,” amesema.
Amesema Serikali imechagua vyuo hivyo kutokana na uwezo wake wa kutoa elimu katika maeneo hayo pamoja na kuwa na ushirikiano na kampuni kubwa za teknolojia, hatua itakayowawezesha wanafunzi kupata uzoefu wa vitendo kabla ya kurejea nchini.

Ameongeza kuwa mpango huo ni endelevu na Serikali tayari imepata nafasi nyingine ya kuwapeleka wanafunzi 10 kusoma nchini Urusi, huku akisisitiza kuwa wataalamu hao wanatarajiwa kuwa chachu ya mabadiliko katika sekta mbalimbali nchini.
Akieleza zaidi kuhusu programu hiyo, Profesa, Steven Maruka amesema wanafunzi hao wamepata ufadhili kupitia mpango wa Samia Scholarship Extended, baada ya kufanya vizuri zaidi katika matokeo ya Kidato cha Sita.

Amesema kabla ya kuanza masomo ya shahada ya kwanza, wanafunzi hao walipitia mafunzo maalumu ya maandalizi kwa kipindi cha takribani miezi 10 ili kuwaandaa kukabiliana na masomo wanayokwenda kusomea.

“Wanaenda kusoma masuala yanayohusiana na Sayansi ya Data, Akili Unde na Sayansi Shirikishi. Hawa ni wanafunzi ambao walikuwa na ufaulu wa juu kuliko wote katika matokeo ya Kidato cha Sita,” amesema.

Profesa huyo amesema kuanzia mwaka wa masomo 2026, Serikali imepanua wigo wa programu hiyo kwa kuanza kufadhili wanafunzi wenye ufaulu wa juu kwenda kusoma nje ya nchi, ikiwa ni mara ya kwanza kwa mpango huo kuwapeleka wanafunzi hao katika vyuo vya nje.

Mwanafunzi: Tumepewa fursa ya kutimiza ndoto

Mmoja wa wanafunzi hao, Angela Mombi, amesema anashukuru Serikali kwa kumpa nafasi ya kuendelea na masomo ya shahada ya kwanza nchini Ireland kupitia mpango huo.

Angela amesema amepata nafasi ya kusoma Shahada ya Sayansi katika chuo kilichopo Ireland, baada ya kumaliza Kidato cha Sita katika Shule ya St. Mary's Mazinde Juu, Tanga.

Amesema fursa hiyo kwake ni hatua kubwa katika kutimiza ndoto zake za kielimu, huku akiahidi kusoma kwa bidii na kutumia elimu atakayoipata kwa manufaa ya Tanzania.
Kwa upande wake, mzazi wa mwanafunzi Sangalu Mahinuka aliyepata fursa hiyo ya kwenda kusoma nje ya nchi, kutoka mkoani Simiyu, Mbogolo Kushaha ameishukuru Serikali kwa kutoa fursa hiyo, akisema inalenga kuandaa wataalamu katika eneo la teknolojia ambalo linaendelea kukua kwa kasi duniani.

Amesema wanafunzi hao wanapaswa kutumia fursa hiyo kujifunza kwa bidii ili watakaporejea nchini waweze kutumia ujuzi na teknolojia watakazozipata katika kutatua changamoto mbalimbali.

Mzazi huyo amewataka wazazi wengine nchini kuwahamasisha watoto wao kusoma kwa bidii ili waweze kutumia fursa za ufadhili zinazotolewa na Serikali na hatimaye kupata ujuzi utakaosaidia maendeleo ya taifa.
DAR ES SALAAM: 
MWANASHERIA Mkuu wa Serikali (AG), Hamza Johari, amesema hatua ya Rais Samia Suluhu Hassan kumpendekeza Deogratius Ndejembi kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kukubaliwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kisha kupitishwa na Bunge kabla ya Septemba 4, 2026, haina changamoto yoyote ya kikatiba wala kisheria.

Johari ametoa ufafanuzi huo Bungeni leo, Agosti 28, 2026, wakati akijibu hoja zilizokuwa zikiibuliwa kuhusu muda wa uteuzi huo, huku baadhi ya watu wakidai kuwa Rais alipaswa kusubiri hadi Septemba 4, 2026 kabla ya kumteua Makamu wa Rais mpya.

Hoja hiyo ilijengwa kwa kurejea barua ya aliyekuwa Makamu wa Rais, Dkt. Emmanuel Nchimbi, ambayo ilieleza kuwa kujiuzulu kwake kungeanza rasmi Septemba 4, 2026, baada ya Rais kukubali ombi hilo.

Hata hivyo, Johari amesema wanaotoa hoja hiyo wamejikita zaidi katika Ibara ya 50(4) ya Katiba bila kuoanisha masharti yake na vifungu vingine, hususan Ibara ya 47 inayoweka masharti kuhusu mtu kushika nafasi ya Makamu wa Rais katika mazingira ambayo hayahusiani na uchaguzi mkuu.

Amesema tafsiri ya Ibara ya 50(4) haiwezi kufanywa kwa kuitazama ibara hiyo pekee, bali inapaswa kuhusishwa na vifungu vingine vya Katiba vinavyoweka masharti ya mtu kuwa na sifa au kupoteza sifa za kushika nafasi ya Makamu wa Rais.

Kwa mujibu wa Johari, miongoni mwa mazingira yanayoweza kusababisha mtu kupoteza sifa ya kushika nafasi hiyo ni pamoja na kupoteza uraia, kutiwa hatiani kwa makosa yanayotajwa na Katiba au kupoteza uanachama wa chama cha siasa.

Amesema katika mazingira ya Dkt. Nchimbi, baada ya CCM kumvua uanachama, tayari alishapoteza sifa ya kuendelea kushika nafasi ya Makamu wa Rais.

Kwa msingi huo, Johari amesema nafasi hiyo ilionekana kuwa wazi, hivyo kumpa Rais mamlaka ya kutumia Ibara ya 50(4) ya Katiba kumteua mtu mwingine bila kusubiri hadi Septemba 4, 2026.

“Suala la kujaza nafasi iliyo wazi ni tofauti na mchakato wa kumchagua Rais na Makamu wa Rais kupitia uchaguzi mkuu,” amesema Johari, akieleza kuwa Katiba imeweka utaratibu maalumu wa kushughulikia nafasi ya Makamu wa Rais inapokuwa wazi.

Amesema utaratibu huo unampa Rais mamlaka ya kupendekeza mtu wa kushika nafasi hiyo, huku uteuzi huo ukiwasilishwa Bungeni kwa ajili ya kuthibitishwa kwa mujibu wa Katiba.

Mwanasheria Mkuu amewataka wanasheria na wananchi wanaojadili masuala ya kikatiba kuzingatia Katiba kwa ujumla wake wakati wa kutoa tafsiri ya vifungu vyake, badala ya kutumia ibara moja pekee kujenga hoja ya kisheria.

Amesisitiza kuwa vifungu vya Katiba vinapaswa kusomwa na kutafsiriwa kwa kuzingatia uhusiano wake na vifungu vingine, hasa pale vinapohusu sifa, madaraka na namna ya kujaza nafasi za viongozi wa kitaifa.

Ufafanuzi huo umeondoa hoja zilizokuwa zimeibuliwa kuhusu uhalali wa muda ambao Rais Samia alimpendekeza Ndejembi kushika nafasi ya Makamu wa Rais kabla ya tarehe Septemba 4, 2026.

Na Belinda Joseph – Dodoma

Walimu wenye ulemavu mkoani Dodoma wamepatiwa elimu ya fedha, uwekezaji na hifadhi ya jamii ili kuwajengea uwezo wa kusimamia kipato, kuwekeza na kujiandaa kwa maisha baada ya kustaafu, mafunzo hayo yameandaliwa na Chama cha Walimu Tanzania (CWT) kwa kushirikiana na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF).

Akizungumza katika mafunzo hayo, Afisa Elimu  Mkoa wa Dodoma Mwalimu Kiduma Mageni, wakati akimwakilisha Katibu Tawala wa Mkoa, amesema elimu ya fedha ni muhimu kwa watumishi kwa kuwa inawasaidia kupanga matumizi, kuweka akiba na kuwekeza, akisisitiza kuwa changamoto za kifedha haziwezi kutatuliwa kwa kuongeza kipato pekee bila kuwa na uelewa wa kukisimamia.

Mwalimu Kiduma amesema walimu wanapaswa kuanza kujiandaa kwa maisha ya baada ya kustaafu mapema kwa kufanya maamuzi sahihi kuhusu matumizi, akiba na uwekezaji ili kuepuka changamoto za kifedha wanapomaliza utumishi.

Kwa upande wake, mwakilishi wa Katibu Mkuu wa CWT, Alfred Alexander, amesema mafunzo hayo yamelenga pia kuwaandaa walimu kukabiliana na maisha baada ya kustaafu, akieleza kuwa baadhi ya wastaafu wamekuwa wakipoteza mafao yao kutokana na kuingia kwenye uwekezaji bila kuwa na uelewa wa kutosha.

Alfred amesema CWT imeialika Mwalimu Commercial Bank kutoa elimu kuhusu fursa za kifedha na uwekezaji, ili kuwasaidia walimu kuanza uwekezaji wakiwa bado kazini na kujenga vyanzo vya ziada vya kipato.

Mkuu wa Idara inayohudumia Walimu Wenye Ulemavu wa CWT, Mwalimu Robert Bundala Katuba, amesema mafunzo hayo yamewapa walimu uelewa kuhusu mabadiliko ya sheria za mifuko ya hifadhi ya jamii pamoja na fursa za uwekezaji, huku akizitaka taasisi nyingine kuunga mkono juhudi za kuwawezesha walimu wenye ulemavu.

Mwalimu Robert amesema CWT inathamini ushirikiano na NSSF katika kutoa elimu hiyo na kwamba maarifa yanayopatikana yanapaswa kuwafikia walimu wengine pamoja na jamii, hususan kuhusu umuhimu wa kujiunga na mifuko ya hifadhi ya jamii na kutumia fursa zinazopatikana.

Meneja wa NSSF Mkoa wa Dodoma amesema mfuko huo utaendelea kushirikiana na CWT kutoa elimu ya hifadhi ya jamii kwa wananchi, akieleza kuwa elimu hiyo ni muhimu katika kuwasaidia kuelewa huduma zinazotolewa na NSSF na fursa zinazopatikana kupitia hifadhi ya jamii.

Mafunzo hayo yameweka mkazo katika umuhimu wa walimu wenye ulemavu kuwa na uelewa wa fedha, uwekezaji na hifadhi ya jamii mapema, ili kuwawezesha kufanya maamuzi sahihi ya kifedha, kujenga vyanzo vya ziada vya kipato na kuwa na maisha yenye utulivu wakati wa utumishi na baada ya kustaafu.





Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Mhe. Abdallah Mitawi, ametembelea Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) kwa lengo la kufahamu kwa kina majukumu ya Mamlaka pamoja na utekelezaji wa shughuli mbalimbali zinazolenga kusimamia na kuendeleza sekta ya usafiri wa anga nchini.

Katika ziara hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa TCAA, Dkt. Jabiri Bakari, alimueleza Naibu Katibu Mkuu kuhusu majukumu na shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na Mamlaka, ikiwemo usimamizi na udhibiti wa shughuli za usafiri wa anga, usalama na ulinzi wa anga, pamoja na utoaji wa huduma kwa watumiaji wa sekta hiyo.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mhe. Mitawi ameipongeza TCAA kwa juhudi inazofanya katika kuhakikisha usalama na ufanisi wa shughuli za usafiri wa anga nchini, akisisitiza umuhimu wa kuendelea kuimarisha usalama wa Usafiri wa anga kwa kuwa sekta hiyo ni kichocheo muhimu cha ukuaji wa uchumi na maendeleo ya Taifa.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa Tanzania kutumia kikamilifu fursa zilizopo katika sekta ya usafiri wa anga, huku akihimiza kuendelea kuboresha huduma na miundombinu, kuimarisha ushirikiano na wadau pamoja na kutumia ubunifu na teknolojia za kisasa ili kuongeza mchango wa sekta hiyo katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Katika ziara hiyo, Mhe. Mitawi pia alitembelea maeneo mbalimbali ya TCAA na kujionea shughuli zinazotekelezwa na Mamlaka, ikiwemo Kituo cha TCAA cha Uongozaji Ndege katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA).

Imeelezwa ziara hiyo ni sehemu ya jitihada za Wizara ya Uchukuzi za kufuatilia utekelezaji wa majukumu na miradi ya kimkakati katika sekta ya usafiri wa anga, kwa lengo la kuhakikisha sekta hiyo inaendelea kukua, kuwa salama na kutoa huduma zenye ufanisi kwa wananchi na wadau mbalimbali.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Bw. Abdallah Mitawi akipokea zawadi kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Dkt. Jabiri K. Bakari alipotembea katika ofisi za Mamlaka zilizopo eneo la Banana, jijini Dar es Salaam.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Bw. Abdallah Mitawi akizungumza na baadhi ya watumishi wa TCAA wakiongozwa na Mkurugenzi Mkuu wa TCAA, Dkt. Jabiri K. Bakari alipotembea ofisi za Mamlaka hiyo eneo la Banana, jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Dkt. Jabiri K. Bakari akitoa taarifa kuhusu kazi zinazofanywa na Mamlaka hiyo kwa Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Bw. Abdallah Mitawi alipotembea katika ofisi za Mamlaka zilizopo eneo la Banana, jijini Dar es Salaam.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Bw. Abdallah Mitawi akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya Menejimenti ya TCAA ikiongozwa na Mkurugenzi Mkuu TCAA, Dkt. Jabiri K. Bakari pamoja na baadhi ya watumishi wa wizara ya Uchukuzi.

Na Mwandishi Wetu, Morogoro

Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA) umeeleza kuwa Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja umeendelea kuhakikisha Tanzania inapata bidhaa za mafuta kwa uhakika, kwa wakati na kwa gharama shindani.

Akizungumza katika Maonesho ya Nne ya Kitaifa ya Utamaduni yanayoendelea mkoani Morogoro, Mchumi wa PBPA, Bw. Henry Kilenga, amesema mfumo huo unahusisha ukusanyaji wa mahitaji ya mafuta kutoka kwa kampuni za uuzaji wa mafuta nchini kabla ya kutangazwa kwa zabuni za kimataifa.

Amesema PBPA hukusanya mahitaji hayo na kuyaunganisha ili mafuta yaagizwe kwa pamoja kwa kiwango kikubwa. Utaratibu huo huiwezesha nchi kunufaika na ununuzi wa pamoja na kupata gharama shindani za uagizaji na usafirishaji.

“PBPA hukusanya mahitaji ya mafuta kutoka kwa kampuni za uuzaji wa mafuta, huandaa zabuni na kuwashindanisha wazabuni waliokidhi vigezo. Utaratibu huu unasaidia kuhakikisha nchi inapata mafuta kwa uhakika na kwa gharama shindani,” amesema Kilenga.

Amefafanua kuwa zabuni hizo hushirikisha kampuni za kimataifa zilizohakikiwa na kukidhi vigezo vilivyowekwa na PBPA. Wazabuni hushindanishwa kwa uwazi, huku tathmini ikizingatia bei zilizowasilishwa, uwezo wa kusambaza mafuta na masharti mengine ya zabuni.

Kwa mujibu wa Kilenga, baada ya kukamilika kwa tathmini, kampuni zilizokidhi vigezo na kuwasilisha bei nzuri huchaguliwa kuleta mafuta nchini kulingana na kiasi na muda uliopangwa.

Kilenga amesema uwazi na ushindani katika uendeshaji wa zabuni unalenga kulinda maslahi ya taifa, kuongeza ufanisi na kuhakikisha bidhaa za mafuta zinaendelea kupatikana kwa ajili ya wananchi na shughuli mbalimbali za kiuchumi.

Amesisitiza kuwa Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja una mchango mkubwa katika kuimarisha usalama wa upatikanaji wa nishati na kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.

Top News