Natumai hujambo Mama yangu, na unaendelea vema na majukumu yako mazito ya kuliongoza na kulijenga Taifa letu la Tanzania. Najua dhamana uliyonayo si ndogo, na najua kila siku mbele yako inakuja na majukumu, matarajio na wakati mwingine changamoto zinazohitaji hekima, uvumilivu na moyo wa ziada.
Mama Rais Samia, waswahili wanasema, “barua ni nusu ya kuonana.” Nami nimeona nikutumie barua hii ya wazi, nikitumaini maudhui yake uyapokee kama vile unavyomuona mwanao anayeketi mbele yako na kukuambia yaliyo moyoni mwake. Siandiki kwa nia ya kukufundisha uongozi, kwa sababu najua dhamana uliyonayo na uzoefu unaokufanya uwe ulipo leo. Naandika kwa sababu mimi ni Mtanzania ninayependa kuona nchi yangu ikiendelea kusonga mbele.
Mama Rais Samia, nimetafakari sana yote yaliyotokea, yanayoendelea kutokea na hata yale tunayodhani yanaweza kutokea huko mbele. Nimetafakari kuhusu taifa letu, kuhusu uongozi wako, kuhusu changamoto zinazojitokeza na kuhusu matarajio makubwa waliyonayo Watanzania. Ghafla, nikajikuta nimekaa mezani, kalamu ikiwa mkononi, nikaanza kukuandikia barua hii ya wazi.
Mama Rais Samia, huenda barua hii isiwe na muhuri wa Serikali, isiwe na nembo ya taasisi yoyote na wala isiwe na cheo chochote nyuma ya jina langu. Lakini ina kitu kimoja muhimu: ina moyo wa Mtanzania anayekuandikia kiongozi wake kwa heshima, kwa nia njema na kwa matumaini kwamba ujumbe huu utakufikia.
Mama Rais Samia, najua kipindi hiki si rahisi. Najua katika safari ya uongozi kuna nyakati ambazo mambo huenda kama ulivyopanga, lakini pia kuna nyakati ambazo matukio huja ghafla na kulazimisha kiongozi kutafakari upya hatua zinazofuata. Ndiyo maana nimeona nikufikishie ujumbe huu mmoja muhimu: Usikate tamaa, Mama. Endelea kujenga nchi yetu.
Rais wangu Dkt. Samia, katika siasa na uongozi, kuondoka kwa mtu mmoja hakupaswi kuwa sababu ya safari ya taifa kusimama. Watu huja na kuondoka, nafasi hubadilika na nyakati hubadilika, lakini nchi hubaki. Tanzania bado ipo, Watanzania bado wana matumaini na mbele yako bado kuna kazi kubwa ya kulijenga taifa hili.
Rais wangu Dkt. Samia, si kila hatua ya uongozi huwa nyepesi. Kuna nyakati ambazo kiongozi hukutana na changamoto zisizotarajiwa, mabadiliko ya kisiasa na maamuzi ya watu aliokuwa akifanya nao kazi kwa karibu. Hayo ni sehemu ya safari ya uongozi, na katika nyakati kama hizi, kinachohitajika zaidi ni utulivu wa akili, hekima na uwezo wa kuangalia mbele.
Rais wangu Dkt. Samia, tunafahamu kwamba kipindi hiki si cha kawaida baada ya Makamu wako Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi, kutangaza kujiuzulu nafasi hiyo. Lakini tukio hilo lisikufanye uone kama safari ya Serikali yako imepata mwisho. Badala yake, lichukulie kama sehemu ya changamoto za uongozi na sababu ya kuongeza nguvu katika kusimamia majukumu uliyopewa na Watanzania.
Rais wangu Dkt. Samia, usife moyo. Usiruhusu changamoto za kisiasa zikupunguzie kasi ya kazi ya kulijenga taifa. Endelea kuwa mtulivu, sikiliza sauti mbalimbali, tafakari kwa kina na chukua maamuzi yenye maslahi mapana ya Tanzania. Wakati mwingine, uimara wa kiongozi hauonekani wakati mambo yako sawa; huonekana zaidi pale anapokutana na mawimbi.
Rais wangu Dkt. Samia, una dhamana kubwa mbele ya Watanzania. Ulipoomba ridhaa yao katika uchaguzi mkuu wa Oktoba, 2025, uliwaahidi mambo mbalimbali kuhusu mustakabali wa nchi yao. Sasa wananchi wanataka kuona ahadi hizo zikigeuka kuwa matokeo. Kazi iliyopo mbele yako si kuangalia sana nani ameondoka au nani amebaki, bali kuhakikisha Tanzania inaendelea kusonga mbele.
Rais wangu Dkt. Samia, ongeza juhudi katika uchumi, ajira, elimu, afya, kilimo, miundombinu na uwekezaji. Lakini zaidi ya yote, endelea kuangalia maisha ya Mtanzania wa kawaida anayehangaika kutafuta chakula, mzazi anayesubiri huduma bora za afya kwa familia yake, kijana anayehitaji ajira na mfanyabiashara anayehitaji mazingira rafiki ya kufanya biashara.
Rais wangu Dkt. Samia, endelea kusikiliza wananchi. Nguvu kubwa ya Serikali haipo katika ofisi kubwa wala magari ya misafara; ipo katika uwezo wa kusikia kilio cha wananchi na kukifanya kuwa sehemu ya ajenda ya Serikali kama ufanyavyo wewe. Wananchi wanahitaji kuona kwamba uongozi wao unawasikia, unawajali na unafanya kazi kwa ajili yao.
Rais wangu Dkt. Samia, Tanzania ni kubwa kuliko mtu mmoja, nafasi moja au tukio moja la kisiasa. Serikali ina taasisi, ina mifumo na ina watendaji. Kwa hiyo, mabadiliko katika nafasi moja yasiruhusiwe kuvuruga mwelekeo wa taifa. Kazi ya Serikali lazima iendelee, miradi iendelee, uchumi uendelee na huduma kwa wananchi ziendelee kuboreshwa.
Rais wangu Dkt. Samia, uongozi hupimwa zaidi wakati wa changamoto kuliko wakati mambo yanapokuwa rahisi. Hiki kinaweza kuwa kipindi kigumu, lakini pia kinaweza kuwa nafasi muhimu kwako kuonyesha zaidi uwezo wako wa kiuongozi, uvumilivu, hekima na weledi katika kuliongoza taifa letu.
Rais wangu Dkt. Samia, Watanzania wanahitaji amani, utulivu na mazingira yatakayowawezesha kufanya kazi na kujenga maisha yao. Wanahitaji kuona tofauti za kisiasa hazigeuki kuwa kikwazo cha maendeleo. Wanahitaji kuona taasisi za Serikali zikifanya kazi kwa ufanisi na viongozi wakitumia madaraka yao kwa ajili ya maslahi ya wananchi.
Rais wangu Dkt. Samia, usikubali changamoto ya leo ikufanye usahau wajibu wa kesho. Historia ya uongozi haijengwi kwa namna kiongozi anavyokabiliana na siku nzuri pekee, bali pia kwa namna anavyosimama imara wakati wa misukosuko na kuhakikisha taifa halianguki.
Rais wangu Dkt. Samia, endelea na kazi. Jenga Tanzania. Timiza yale uliyowaahidi Watanzania. Ongeza maarifa, hekima, juhudi na weledi. Wakati huu unahitaji uongozi unaotazama mbele, unaotanguliza taifa na unaojua kwamba dhamana uliyonayo ni kubwa kuliko changamoto yoyote ya kisiasa inayoweza kujitokeza.
Rais wangu Dkt. Samia, changamoto zitapita, watu watabadilika na nyakati zitabadilika, lakini Tanzania itaendelea kubaki. Kinachohitajika sasa ni uongozi wenye utulivu, hekima, uadilifu, uwajibikaji na maono ya mbali.
Rais wangu Dkt. Samia, huu ndiyo wakati wa kuangalia mbele zaidi kuliko nyuma. Huu ndiyo wakati wa kuimarisha timu yako, kusimamia kwa karibu utekelezaji wa mipango ya Serikali na kuhakikisha kila ahadi iliyotolewa kwa wananchi inapata majibu katika vitendo.
Rais wangu Dkt. Samia, ujumbe wangu kwako ni mmoja tu: Usikate tamaa. Jenga nchi. Endelea kufanya kazi kwa ajili ya Watanzania. Tanzania inahitaji uongozi unaotazama mbele.
Ni mimi mwanao Rashid Mtagaluka
Mbagala, Dar es Salaam
28/08/2026
Simu: 0718 406 242
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amewasili leo, tarehe 30 Agosti 2026, jijini Belgrade, Jamhuri ya Serbia, kumwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Mkutano Maalum wa Ngazi ya Juu wa Kumbukumbu ya Miaka 65 tangu kufanyika kwa Mkutano wa Kwanza wa Wakuu wa Nchi wa Harakati za Nchi Zisizofungamana na Upande Wowote (NAM).
Rais Dkt. Mwinyi amewasili akiwa ameambatana na ujumbe wake, akiwemo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo, pamoja na viongozi wengine wa Serikali.
Katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Nikola Tesla, Rais Dkt. Mwinyi amepokelewa na Naibu Waziri Mkuu ambaye pia ni Waziri wa Uchumi wa Jamhuri ya Serbia, Mhe. Adrijana Mesarović, pamoja na Balozi wa Tanzania nchini Italia ambaye pia anaiwakilisha Tanzania katika Jamhuri ya Serbia, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk.
.jpeg)
Dkt. Mwigulu ameyasema hayo leo Jumapili, Agosti 30, 2026, katika maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 25 ya Jimbo Katoliki la Mpanda, yaliyofanyika mkoani Katavi, ambapo amesema Serikali inatambua mchango wa Kanisa Katoliki katika maendeleo ya nchi, hususan katika sekta za elimu, afya na huduma za kiroho.
“Serikali inatambua mchango wa Kanisa na baba Askofu. Kila tunapotaja maendeleo ya nchi yetu, kuanzia mwanzo mpaka hapa tulipofika, hatuwezi kuyataja kwa kina maendeleo hayo bila kutaja mchango wa Kanisa.”
Amesema ushirikiano kati ya Serikali na Kanisa umeendelea kuwa muhimu katika kuhakikisha huduma za kijamii na shughuli za maendeleo zinaimarika, akisisitiza kuwa milango ya Serikali itaendelea kuwa wazi kwa Kanisa na taasisi nyingine za dini katika masuala yanayolenga ustawi wa wananchi.
“Niwahakikishie Serikali itaendelea kushirikiana na Kanisa na popote pale mlipo na jambo msisite, milango yetu iko wazi ili tuweze kuhakikisha kwamba tufanye jambo lolote linalotufurahisha.”
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ametoa maelekezo kwa viongozi wa Mkoa wa Katavi na mamlaka husika kuharakisha utekelezaji wa miradi ya barabara, maji na umeme, akisisitiza kuwa wananchi wanapaswa kupata huduma hizo kwa wakati.
Amesema maandalizi ya kukabiliana na uwezekano wa kutokea kwa El Niño yanapaswa kwenda sambamba na hatua za vitendo, ikiwemo ujenzi na uboreshaji wa mifereji na madaraja ili kupunguza athari za mafuriko.
Kuhusu huduma za maji, Waziri Mkuu ameitaka Wizara ya Maji na wahusika wa mradi wa maji Mpanda kuhakikisha wananchi wanapata huduma hiyo ifikapo Desemba 2026, huku akisisitiza pia kuharakishwa kwa miradi ya barabara inayounganisha Katavi na mikoa jirani.
Aidha, Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea kuchukua hatua za kuboresha mazingira ya haki kwa wananchi, akitangaza kuwa Serikali inaelekea kufuta sheria inayohusu utaifishaji wa mifugo, akieleza kuwa hatua hiyo inalenga kuondoa changamoto za wananchi kunyang’anywa mifugo yao.
“Katika Bunge hili linaloendelea tunakwenda kufuta sheria ya utaifishaji wa mifugo... kumekuwepo na majeraha makubwa ya watu kunyang’anywa katika baadhi ya maeneo. Tunataka tuondoe hayo ili kuhakikisha kwamba wananchi wetu wanaepukana na hayo.”
Pia ametoa maelekezo kwa wasimamizi wa sheria kuacha kukamata vitendea kazi vya wananchi kama pikipiki, bajaji na magari katika utekelezaji wa sheria za makosa mbalimbali, akisisitiza umuhimu wa kutumia utaratibu wa kisheria wa adhabu na faini.
Kwa upande wake, Askofu wa Jimbo Katoliki la Mpanda, Mhashamu Baba Askofu Eusebius Nzigilwa, amemshukuru Waziri Mkuu kwa kutenga muda na kushiriki katika maadhimisho hayo, akisema uwepo wake umeonesha heshima na kuthaminiwa kwa Jimbo la Mpanda na Kanisa Katoliki Tanzania.
“Ninakushukuru sana. Tunaona hiyo ni heshima kwa Jimbo letu na kwa Kanisa Katoliki Tanzania, na hivyo tunaomba Mwenyezi Mungu azidi kuwaongoza na kuwajalia neema na hekima katika kutuongoza sisi raia na wananchi wenu.”
Naye Balozi wa Baba Mtakatifu nchini Tanzania anayemaliza muda wake, Mhashamu Askofu Mkuu Angelo Accattino, amesisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano kati ya Serikali na Kanisa Katoliki, akisema ushiriki wa viongozi wa Serikali na viongozi wa dini mbalimbali katika maadhimisho hayo ni ishara ya mahusiano mema kwa ajili ya ustawi wa jamii.
Maadhimisho hayo yamefanyika katika kuadhimisha miaka 25 tangu kuanzishwa kwa Jimbo Katoliki la Mpanda mwaka 2001, huku viongozi wa Kanisa wakieleza kuwa katika kipindi hicho Jimbo limepiga hatua katika huduma za kichungaji, elimu, afya na ujenzi wa miundombinu kwa ajili ya jamii.
Waziri Mkuu amewapongeza viongozi wa Kanisa, waamini na wananchi wa Jimbo Katoliki la Mpanda kwa kufanikisha Jubilee hiyo, akiwataka kuendelea kushirikiana na Serikali katika kujenga jamii yenye amani, mshikamano na maendeleo.

.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)








.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)





















.jpeg)



.jpeg)