Msanii na mtayarishaji wa filamu nchini   na Diwani wa Viti Maalum Wilaya ya Kinondoni, Councillor Lilian Shirima "Manka amesema amewahi kukutana na changamoto ya kushinikizwa kufanya ngono ili apewe nafasi za kuigiza, akieleza kuwa hali hiyo iliwahi kuwa miongoni mwa vikwazo vilivyowakabili waigizaji wanawake katika safari ya kutafuta ajira kwenye sekta ya sanaa. 

Hayo ameyasema wakati wa uzinduzi wa Tamthiliya yake mpya iitwayo “Mbalamwezi” inayorushwa kwenye king’amuzi cha Azam  ambaoi amesema waigizaji wanafanya kazi ili kujipatia kipato na kusaidia familia zao, hivyo haikuwa sahihi kutumia nafasi za kazi kama njia ya kuwanyonya.

Amesema changamoto hiyo ilimkuta mara kadhaa, ambapo baada ya kufanya casting na kuonesha uwezo wake, baadhi ya watu waliokuwa na mamlaka ya kutoa nafasi walimuita katika mazingira binafsi na kuanza kutoa masharti yasiyohusiana na kazi. 

“Unakuta unaenda, unapewa casting, unatoa scene tatu au nne, lakini mwisho wa siku producer anakuita na kuanza kukwambia mambo mengine. Sasa ni wewe kukubali au kukataa. Ukikataa, huyo mtu anakasirika na casting zako zinachukuliwa na kupewa mtu mwingine,” amesema.

Hata hivyo, amesema hali ya sasa inaweza kuwa tofauti kutokana na kukua kwa soko la sanaa, kuongezeka kwa maproducer na kuwepo kwa fursa nyingi zaidi kwa wasanii. 

Amesema changamoto hizo zilimjengea nguvu ya kufanya kazi kwa bidii na kumuomba Mungu ili kufanikiwa bila kutegemea mtu mmoja. 

“Ilinipa focus sana kufanya kazi kwa bidii ili na mimi niweze kufanya kazi yangu. Ilinishawishi niwe mwombaji sana, nikamwomba Mungu sana, ili ule mtu ajue kwamba bila yeye pia kuna Mungu,” amesema.

Akizungumzia uzoefu wake wa kufanya kazi na Azam, amesema si rahisi kupata nafasi ya kuingiza kazi katika kituo hicho, bali kinachoweza kumsaidia mtayarishaji ni kuwa na kazi yenye ubora, maudhui ya Kitanzania na Afrika pamoja na kuzingatia maadili. 

Amesema kazi hupitia mchakato mkali wa uchambuzi wa maudhui kabla ya kuidhinishwa, huku script, uzalishaji, lugha, mavazi na masuala mengine yakizingatiwa. “Azam wanataka story yenye maudhui ya Afrika, maudhui ya Tanzania. Wanazingatia maadili, kuanzia maneno, matamshi, mavazi na muonekano wa mtu,” amesema.

Aidha, amewashauri watayarishaji chipukizi kutokata tamaa, bali kujenga kampuni zilizosajiliwa na kufuata taratibu za kisheria, huku wakihakikisha wana timu yenye weledi na vifaa vyenye ubora. Amesema mafanikio katika sekta hiyo yanahitaji maandalizi, ubunifu na uzalishaji bora. “Unaweza ukaproduce kazi nzuri lakini ukakosa mtu wa kukushika mkono. Kwanza lazima uwe na kampuni, uisajili BRELA na kufuata taratibu zinazohitajika. Lakini pia production yako iwe imesimama na crew yako iwe na watu wanaojua wanachotakiwa kufanya,” amesema.














 


Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Kikodi Ilala imefanya kikao na Washauri wa Kodi ambapo pande hizo mbili zimeeleza azma ya kuendelea kushirikiana katika kuwaelimisha walipakodi haki na wajibu wao. 

Akizungumza katika kikao hicholeo Agosti, 18 2026, jijini Dar es Salaam, Meneja TRA Ilala, Musibu Shabani amesema kuwa TRA inatambua nafasi ya washauri wa kodi katika kuwasaidia wafanyabiashara kutimiza wajibu wao wa kikodi. 

Aidha amewasisitiza kuendelea kushirikiana na TRA katika kuwajengea walipakodi uelewa wa haki walizonazo pamoja na wajibu wao wa kikodi. 

“Mbali na kuwa wateja wenu, wafanyabiashara pia ni walipakodi wanaotegemewa katika kuijenga nchi. Kama wataalamu, tunapaswa kushirikiana katika kuwawezesha kutimiza wajibu wao ili ulipaji wa kodi usiwe mzigo kwao,” amesema Shabani.  

Ameongeza kuwa milango ya TRA iko wazi katika kuhakikisha changamoto zote za kikodi zinazowakumba washauri wa kodi na wateja wao zinatatuliwa na kuwaahidi huduma bora. 

Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Washauri wa Kodi Tanzania (TATC) Sospeter Kibishi ameahidi kwa niaba ya washauri hao kuwa wataendelea kushirikiana na TRA kutoa elimu na kuimarisha uhusiano ili kuweka mazingira mazuri ya ulipaji wa kodi nchini.







Na  Mandishi Wetu


MAMLAKA ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imeteketeza ekari 603 za mashamba ya bangi na kukamata magunia 49 ya bangi katika operesheni maalum iliyofanyika Wilaya ya Mvomero, mkoani Morogoro, huku watuhumiwa 13 wakikamatwa  kuhusisiana na mashamba hayo. 

Operesheni hiyo iliyofanyika katika vijiji vya Misengele, Lugenge, Kisaki na Nyarutanga, pia ilibaini na kuharibu kambi 21 zilizokuwa zikitumiwa na wakulima wa bangi.

Akizungumza kuhusu operesheni hiyo, Kamishna Jenerali wa DCEA Aretas Lyimo, amesema hatua hiyo ni sehemu ya mkakati endelevu wa Serikali wa kudhibiti uzalishaji wa dawa za kulevya nchini, hususan bangi, ambayo imeendelea kuzalishwa katika baadhi ya maeneo ya nchi.

Amesema operesheni hizo zimebaini mabadiliko katika mbinu zinazotumiwa na baadhi ya wakulima wa bangi, ambapo wanahamisha shughuli zao kutoka maeneo yaliyofikiwa na operesheni na kuingia ndani zaidi ya maeneo ya hifadhi.

“Tumebaini kuwa baadhi ya wakulima wamehamishia shughuli zao ndani zaidi ya maeneo ya hifadhi ili kukwepa hatua za kisheria. Hali hii inachangia uharibifu mkubwa wa mazingira kupitia ukataji wa miti ovyo, uvamizi wa vyanzo vya maji na kuathiri mfumo wa ikolojia,” amesema Lyimo.

Kwa mujibu wa Lyimo, tathmini ya operesheni zilizotekelezwa na DCEA tangu mwaka 2023 imeonyesha kuwa, licha ya mashamba mengi ya bangi kubainika na kuteketezwa katika Mkoa wa Morogoro, baadhi ya wahusika wameendelea kubadilisha maeneo ya uzalishaji na kujificha ndani ya maeneo ya hifadhi.

Amesema hali hiyo inahitaji ushirikiano wa karibu zaidi kati ya DCEA, vyombo vya ulinzi na usalama, mamlaka zinazosimamia maeneo ya hifadhi na wananchi ili kuzuia maeneo hayo kutumiwa kwa uzalishaji wa dawa za kulevya.

Lyimo amewataka wasimamizi wa maeneo ya hifadhi kuhakikisha maeneo wanayoyasimamia hayatumiki kwa kilimo cha bangi, akisisitiza kuwa mapambano dhidi ya uzalishaji wa dawa za kulevya yanahitaji ushirikiano wa taasisi na jamii.

DCE itaendelea kufanya operesheni jumuishi katika maeneo mbalimbali nchini kwa kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama, mamlaka za uhifadhi na wananchi ili kudhibiti kilimo na biashara haramu ya bangi.

Sambamba operesheni hizo, Lyimo amesema Mamlaka itaendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu madhara ya dawa za kulevya na kuhamasisha wananchi kutoa taarifa kuhusu watu wanaojihusisha na uzalishaji, usafirishaji na biashara haramu ya dawa za kulevya.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Uwanja wa AFCON unaojengwa Fumba utakuwa uwanja wa kisasa wenye hadhi ya kimataifa na chachu ya kufungua fursa mbalimbali kwa wananchi.

Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, 18 Agosti 2026, wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa Uwanja wa AFCON pamoja na Bandari ya Fumba, Mkoa wa Mjini Magharibi.

Amesema kukamilika kwa uwanja huo kutaiweka Zanzibar katika nafasi nzuri ya kunufaika na fursa za biashara, huduma na shughuli nyingine za kiuchumi zitakazotokana na ongezeko la wageni, hususan wakati wa Michuano ya AFCON 2027.

Rais Dkt. Mwinyi amesema Serikali itaendelea kuhakikisha miundombinu inayozunguka uwanja huo inajengwa kwa ubora na viwango vinavyokubalika kimataifa, ili kuongeza thamani ya eneo hilo na kuleta tija kwa Zanzibar kwa muda mrefu.

Kwa sasa, ujenzi wa Uwanja wa AFCON umefikia takribani asilimia 80, huku miundombinu mbalimbali ikiendelea kujengwa, ikiwemo barabara ya kisasa itakayoboresha usafiri na kuongeza haiba ya eneo hilo.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amesema Serikali inaendelea kujenga viwanja vya michezo katika maeneo mbalimbali ya Zanzibar kwa lengo la kukuza vipaji vya vijana na kuwawezesha kupata fursa za kushiriki mashindano ya kitaifa na kimataifa.

Ameipongeza Kampuni ya Orkun kwa utekelezaji wa ujenzi wa uwanja huo kwa kuzingatia ubora na hadhi ya kimataifa, pamoja na kuweka miundombinu inayouwezesha kuhudumia shughuli mbalimbali za michezo na kijamii.

Uwanja wa AFCON Fumba utakuwa na uwezo wa kuchukua watazamaji 36,500, pamoja na viwanja viwili vya nje vyenye uwezo wa kuchukua watazamaji 5,000 kila kimoja.

Uwanja huo unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa Desemba 2026, ikiwa ni sehemu muhimu ya maandalizi ya Zanzibar kuelekea AFCON 2027.















Na Karama Kenyunko, Michuzi TV

MAMLAKA ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa tahadhari ya kuwepo kwa mvua za El Nino zitakazoathiri msimu wa mvua za Vuli unaotarajiwa kuanza mapema Oktoba 2026 na kuendelea hadi Januari 2027.

Akizungumza na waandishi wa habari, leo Agosti 18, 2026 Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dkt. Ladislaus Chang’a, amesema msimu wa mvua za Vuli 2026 unatarajiwa kuathiriwa kwa kiwango kikubwa na hali ya El Nino yenye nguvu kubwa, huku mvua za juu ya wastani hadi wastani zikitarajiwa katika maeneo mengi.

Amesema mvua hizo zinatarajiwa kuanza wiki ya nne ya Septemba hadi wiki ya kwanza ya Oktoba 2026 katika maeneo ya Ukanda wa Ziwa Victoria na baadaye kusambaa katika maeneo mengine mwezi Oktoba.

Amesema mvua za juu ya wastani hadi wastani zinatarajiwa katika Kanda ya Ziwa Victoria, ikijumuisha Kagera, Geita, Mwanza, Shinyanga, Simiyu na Mara, pamoja na kaskazini mwa Mkoa wa Kigoma.

Aidha, mvua hizo zinatarajiwa katika Dar es Salaam, Tanga, Pwani ikiwemo Mafia, kaskazini mwa Morogoro, Unguja na Pemba, pamoja na Arusha, Manyara na Kilimanjaro.

Dkt. Chang’a amesema kwa kawaida mvua za Vuli huisha mwezi Desemba, lakini katika msimu huu mvua za nje ya msimu zinatarajiwa kuendelea hadi Januari 2027, huku ongezeko la mvua likitarajiwa katika mwezi Novemba 2026.

Amesema vipindi vya unyevu kupita kiasi kwenye udongo pamoja na mafuriko vinaweza kujitokeza na kuathiri ukuaji wa mazao na miundombinu ya kilimo, huku magonjwa ya mazao yanayosababishwa na kuvu, bakteria na virusi yakitarajiwa kujitokeza.

“Mvua za muda mrefu zinaweza kuathiri shughuli za uvunaji na kusababisha upotevu wa mazao baada ya kuvuna. Hata hivyo, shughuli za kilimo zinatarajiwa kuendelea kama ilivyo kawaida katika baadhi ya maeneo katika msimu huu wa Vuli, 2026,” amesema.

Aidha, amesema ongezeko la kina cha maji katika mabwawa na mito linatarajiwa kujitokeza, hali ambayo inaweza kuathiri miundombinu ya rasilimali za maji na nishati, huku magonjwa ya mlipuko yakitokea kutokana na uchafuzi wa maji.

Dkt. Chang’a amewataka wakulima kuandaa mashamba, kupanda, kupalilia na kutumia pembejeo husika kwa wakati, pamoja na kutumia mbinu bora za kuzuia maji kutuama shambani, mmomonyoko na upotevu wa rutuba.

Ametoa tahadhari pia kwa wadau wa usafirishaji, akisema hali mbaya ya hewa inaweza kuathiri miundombinu na shughuli za usafirishaji kwa njia za barabara, reli, bandari na viwanja vya ndege, ikiwemo mmomonyoko wa udongo, kuporomoka kwa kingo za barabara, uharibifu wa madaraja na njia za reli za MGR na SGR.

Aidha, amesisitiza wito wa tahadhari kwa wadau wa mifugo na uvuvi, utalii na wanyamapori, nishati na madini, sekta ya afya, Serikali za Mitaa, ujenzi, sekta binafsi pamoja na Menejimenti za Maafa za wilaya, mikoa na kitaifa ili kuendelea kuratibu mipango ya kupunguza madhara yanayoweza kujitokeza.

Mashindano ya 23 ya Shirikisho la Michezo ya Shule za Sekondari Afrika Mashariki (FEASSA) yamepata msukumo mkubwa baada ya Benki ya Maendeleo ya Afrika Mashariki (EADB) kutoa udhamini wa Dola za Marekani 90,000, (takribani mil 240) katika kuunga mkono maandalizi na uendeshaji wa mashindano ya shirikisho hilo yanayoendelea mkoani Morogoro.

Mashindano hayo makubwa zaidi ya michezo ya shule katika ukanda wa Afrika Mashariki yamezikutanisha timu 413 na washiriki 5,548 kutoka nchi mbalimbali za Afrika Mashariki, zinazoshindana katika aina 51 za michezo. Mashindano hayo yanatarajiwa kuhitimishwa Agosti 22, 2026.

Akizungumza katika hafla rasmi ya ufunguzi wa mashindano hayo, Meneja wa EADB nchini Tanzania, Bw. Stephen Wambura, alisema ushirikiano wa Benki hiyo na FEASSA unaakisi dhamira ya EADB ya kuwekeza kwa vijana na kuunga mkono mipango inayochangia maendeleo endelevu katika Afrika Mashariki.

“Ingawa jukumu letu kuu ni kufadhili miradi ya maendeleo katika sekta mbalimbali muhimu za uchumi, tunatambua kuwa maendeleo endelevu hayaishii kwenye miundombinu na shughuli za biashara. Pia yanahusisha kuwawezesha watu, hususan vijana, ambao ndio msingi wa mustakabali wa ukanda wetu,” alisema Bw. Wambura.

Alisema dhamira hiyo ndiyo iliyochochea uamuzi wa EADB kuwa mdhamini mkuu wa Mashindano ya 23 ya FEASSA, kwa kutoa mchango wa Dola za Marekani 90,000 kwa ajili ya kuwezesha mashindano hayo kufanyika kwa mafanikio.

“Udhamini wa michezo ni mojawapo ya nguzo muhimu katika ajenda yetu ya Mipango ya Uwajibikaji wa Kijamii wa Kampuni (CSI), kwa sababu tunaelewa uwezo mkubwa wa michezo katika kujenga tabia, kuhamasisha mtindo bora wa maisha na kufungua fursa kwa vijana katika ukanda wetu,” aliongeza.

“Kupitia udhamini huu, hatuwekezi tu katika mashindano haya, bali pia tunawekeza katika kuwaandaa kizazi kijacho cha viongozi wa Afrika Mashariki.”

Kwa mujibu wa makubaliano ya udhamini, EADB inasaidia utengenezaji wa medali na vikombe kwa ajili ya washindi, pamoja na upatikanaji wa sare za michezo kwa washiriki watakaoshiriki katika hatua za fainali.

Ikiwa mwenyeji wa mashindano ya mwaka huu, Tanzania imetuma moja ya vikosi vikubwa zaidi, ikiwa na timu 127 na washiriki 1,704 wanaoshiriki katika michezo mbalimbali.

Katika mpira wa miguu kwa wavulana, Tanzania inawakilishwa na Shule za Sekondari Nsumba, Mbeya Day, Morogoro na Urambo Day, ambazo zitakuwa na jukumu la kutetea heshima ya nchi katika mashindano hayo.

Kwa upande wa mpira wa miguu kwa wasichana, Tanzania inawakilishwa na Shule za Sekondari Ziba, Fountain Gate na Kilombero, ambazo zinatarajiwa kutumia vyema fursa ya kucheza mbele ya mashabiki wa nyumbani katika kuwania nafasi za juu.

Tanzania pia inalenga kufanya vizuri katika mpira wa wavu. Katika upande wa wavulana, Shule za Sekondari Lumala, Kaliua na Kajunjumele ndizo zinazobeba matumaini ya Tanzania, huku Mengele, Lumala na Mwanhuzi zikiiwakilisha nchi katika mashindano ya wasichana.

Mpira wa kikapu ni miongoni mwa michezo ambayo Tanzania inalenga kutumia vizuri fursa ya kucheza nyumbani. Katika mashindano ya wavulana ya 5x5, Tanzania inawakilishwa na Shule za Sekondari Nsumba, St Jude na Juhudi.

Kwa upande wa wasichana wa 5x5, Shule za Sekondari Orkeeswa, Uru Community na Rungwa ndizo zitakazobeba matumaini ya Tanzania.

Tanzania pia inatarajia kupata matokeo mazuri katika netiboli, mchezo ambao kwa muda mrefu umekuwa miongoni mwa michezo ambayo Tanzania imekuwa ikitoa timu zenye ushindani mkubwa. Shule za Sekondari Mkolani, Vwawa na Mbeya ni miongoni mwa timu zinazotarajiwa kuongoza kinyang’anyiro cha Tanzania katika mchezo huo.

Kwa kuwakutanisha maelfu ya vijana kutoka nchi mbalimbali za Afrika Mashariki, Michezo ya FEASSA haitoi tu jukwaa la ushindani wa kimichezo, bali pia inawapa vijana fursa ya kukuza vipaji, nidhamu, mshikamano, uwezo wa kufanya kazi kwa pamoja na uongozi, huku ikichangia kuimarisha mshikamano na ushirikiano wa kikanda kupitia michezo.

Kadiri mashindano yanavyoelekea kileleni kuelekea tarehe 22 Agosti, Tanzania inalenga kutumia vyema faida ya kuwa mwenyeji ili kujinyakulia medali katika michezo mbalimbali. Kwa upande wake, udhamini wa EADB unaendelea kusisitiza dhamira ya Benki hiyo ya kuunga mkono mipango inayowekeza katika vijana na kuchangia maendeleo ya muda mrefu ya Afrika Mashariki.

Meneja wa Benki ya Maendeleo ya Afrika Mashariki (EADB), Bw. Stephen Wambura (kulia), akikabidhi rasmi sare za michezo kwa Rais wa Shirikisho la Michezo ya Shule za Sekondari Afrika Mashariki (FEASSA), Bw. Justus Mugisha, kwa ajili ya kutumiwa na timu zinazoshiriki katika hatua za fainali za Michezo ya FEASSA zinazoendelea Morogoro, Tanzania. Sare hizo ni sehemu ya udhamini wa Dola za Marekani 90,000 ( takribani mil 240) kutoka EADB kwa ajili ya kufanikisha toleo la 23 la mashindano hayo ya michezo ya shule katika ukanda wa Afrika Mashariki, ambayo yamewakutanisha timu 413 na washiriki 5,548 kutoka nchi mbalimbali za Afrika Mashariki.




Na Janeth Raphael -MichuziTv


Tanzania na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) zimeweka mkazo mpya katika kuimarisha uhusiano wao wa kiuchumi na kimkakati, huku sekta za madini, biashara, uwekezaji na miundombinu zikitajwa kuwa maeneo muhimu ya ushirikiano kati ya mataifa hayo mawili.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema hayo leo Agosti 18, 2026, Ikulu Ndogo Zanzibar, baada ya kumpokea Rais wa DRC, Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo, aliyewasili nchini kwa ziara ya kikazi.

Rais Samia amesema mazungumzo yake na Rais Tshisekedi yamejikita katika namna Tanzania na DRC zinavyoweza kutumia fursa zilizopo katika rasilimali na uchumi wa mataifa hayo kwa manufaa ya wananchi wa nchi zote mbili.

Kwa mujibu wa Rais Samia, sekta ya madini ni miongoni mwa maeneo yenye nafasi kubwa ya kuunganisha Tanzania na DRC, kutokana na utajiri wa rasilimali za madini uliopo katika nchi hizo.

Amesema ushirikiano huo unaweza kuwezesha mataifa hayo kubadilishana uzoefu na utaalamu katika uchimbaji wa madini, uongezaji thamani pamoja na upatikanaji wa masoko, hatua inayoweza kuongeza mchango wa sekta hiyo katika uchumi wa nchi zote mbili.

Katika eneo la biashara na uwekezaji, Rais Samia amesema Tanzania na DRC zimekubaliana kuweka mazingira yatakayorahisisha zaidi shughuli za wafanyabiashara na wawekezaji, ikiwemo kupunguza vikwazo visivyo vya lazima na kuboresha huduma katika maeneo ya mipakani.

Amesema hatua hiyo inalenga kuongeza mzunguko wa bidhaa na huduma kati ya nchi hizo, huku sekta binafsi ikipewa nafasi kubwa zaidi ya kutumia fursa zinazotokana na ushirikiano huo.

Miundombinu pia imepewa uzito katika mazungumzo hayo, ambapo Rais Samia amesema kukamilika kwa ujenzi wa barabara ya Kalemie–Manono kutakuwa na umuhimu mkubwa katika kuimarisha muunganiko wa Tanzania na DRC.

Amesema miundombinu hiyo haitarahisisha tu usafirishaji wa watu na bidhaa, bali pia itafungua zaidi fursa za biashara na kuchochea shughuli za kiuchumi katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Mbali na masuala ya kiuchumi, viongozi hao wamezungumzia pia amani na usalama, huku wakisisitiza umuhimu wa ushirikiano katika kulinda utulivu wa eneo la Afrika na kuweka mazingira bora kwa maendeleo ya wananchi.

Rais Samia amesema Tanzania itaendelea kuwa mshirika wa karibu wa DRC katika juhudi za kujenga uchumi unaowaunganisha wananchi wa mataifa hayo, pamoja na kuendeleza mazingira yatakayowezesha biashara, uwekezaji na maendeleo ya pamoja.

Amesema ziara ya Rais Tshisekedi nchini Tanzania ni fursa ya kuendeleza uhusiano wa kihistoria uliopo kati ya nchi hizo na kuufanya kuwa msingi wa ushirikiano mpana zaidi katika maeneo ya kimkakati.

Kwa hatua hiyo, Tanzania na DRC zimeelekeza nguvu katika kujenga ushirikiano unaokwenda zaidi ya mahusiano ya kidiplomasia, kwa kulenga kuunganisha uchumi, miundombinu, biashara na fursa za uwekezaji kwa manufaa ya wananchi wa pande zote mbili.

Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) Mhe. Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo akisaini Kitabu cha Wageni baada ya kuwasili Ikulu Ndogo ya Zanzibar, tarehe 18 Agosti, 2026.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) Mhe. Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo baada ya kuwasili Ikulu Ndogo ya Zanzibar, tarehe 18 Agosti, 2026.

Na Belinda Joseph-Tanga.

Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) Kanda ya Kaskazini imetumia Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu jijini Tanga kuelimisha wananchi kuhusu matumizi sahihi ya mbolea, ubunifu wa kiteknolojia pamoja na fursa za mbolea ya ruzuku kwa wakulima.

Akizungumza na Michuzi Tv Agosti 18, 2026 katika viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara jijini Tanga, Meneja wa TFRA Kanda ya Kaskazini, Gothard Liampawe, amesema TFRA imejipanga kutumia mashamba ya mfano kuwafundisha wakulima matumizi sahihi ya mbolea ili kuongeza uelewa na tija katika uzalishaji.

Amesema pamoja na elimu kupitia mashamba ya mfano, TFRA imebuni mifumo mbalimbali ya kiteknolojia inayorahisisha utekelezaji wa majukumu yake, ikiwemo Mfumo wa FIS, unaomwezesha mfanyabiashara kujisajili na kuomba leseni ya biashara, kusajili mbolea na kupata vibali vya kusafirisha au kuingiza mbolea nchini bila kufika katika ofisi za TFRA.

“Mfanyabiashara anaweza kutumia kompyuta yake akiwa mahali popote alipo kufanya maombi hayo bila kulazimika kufika ofisini, hivyo tunaokoa muda na gharama za usafiri,” amesema Liampawe.

Amesema ubunifu huo umeipa TFRA fursa ya kushiriki katika Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu jijini Tanga, kwa lengo la kuwaonesha Watanzania hatua iliyofikiwa katika matumizi ya teknolojia na namna inavyoweza kurahisisha huduma mbalimbali.

Liampawe amesema kuelekea msimu mpya wa kilimo, TFRA Kanda ya Kaskazini imejipanga kuimarisha huduma kwa wakulima na watoa huduma katika sekta ya mbolea kwa kuwatembelea wadau na kuhakikisha wanapata huduma bora, huku ikipanua wigo wa elimu kupitia kampeni ya “Mali Shambani, Silaha Mbolea.”

Amesema katika mwaka wa 2025/2026, Kanda ya Kaskazini imesimamia utekelezaji wa mpango wa mbolea za ruzuku ambapo zaidi ya wakulima 650,000 wamejisajili na kuwa tayari kunufaika na mpango huo, huku wakulima 173,000 tayari wakiwa wamenufaika na jumla ya tani 179,000 za mbolea hadi wiki iliyopita.

Ameutaja mkoa wa Kilimanjaro kuwa kinara kwa matumizi ya mbolea za ruzuku katika Kanda ya Kaskazini, ukifuatiwa na Arusha, Manyara na Tanga, huku zaidi ya Shilingi bilioni 80 zikiwa zimetumika katika upatikanaji wa mbolea hizo.

Aidha, Liampawe amewahimiza wakulima ambao tayari wamejisajili kutotumia vibaya fursa hiyo ya ruzuku inayotolewa na Serikali, huku ambao hawajajisajili akiwataka kufanya hivyo ili waweze kunufaika na mpango huo na kuongeza tija katika kilimo.




Na Belinda Joseph-Tanga

Serikali imeanza mchakato wa kutafuta eneo kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha uhakiki wa malori ya mafuta katika Mkoa wa Tanga, hatua inayolenga kuwaondolea wafanyabiashara usumbufu, muda na gharama za kusafiri hadi Mkoa wa Pwani kupata huduma hiyo.

Hayo yameelezwa na Meneja wa Wakala wa Vipimo (WMA) Mkoa wa Tanga, Julius Temba, leo Agosti 18, 2026, wakati akizungumza katika mwendelezo wa Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea jijini Tanga.

Temba amesema mchakato huo umeanza katika mwaka wa fedha 2026/2027 baada ya Serikali kutambua changamoto inayowakabili wafanyabiashara wa malori ya mafuta wanaohitaji huduma ya uhakiki.

Amesema kwa sasa, wafanyabiashara kutoka Tanga hulazimika kusafiri hadi eneo la Misugusugu, Mkoa wa Pwani, kwa ajili ya kuhakiki malori yao, hali inayoongeza gharama na muda wa kupata huduma hiyo.

Amesema kituo hicho kinatarajiwa kujengwa katika eneo litakalokuwa kwenye barabara ya Segera kuelekea Tanga, na kikikamilika kitasaidia kurahisisha huduma ya uhakiki wa malori ya mafuta kwa wafanyabiashara wa Tanga na maeneo jirani.

Amesema bado kuna changamoto ya baadhi ya watu kutumia vipimo visivyo sahihi, hivyo Wakala unaendelea kutoa elimu na kuimarisha ufuatiliaji ili kuhakikisha wananchi wanatumia vipimo vinavyokidhi viwango vinavyotakiwa.

Amesema kupitia maonesho hayo, WMA inalenga kuwafikia wananchi wengi zaidi na kuwaelimisha kuhusu umuhimu wa vipimo sahihi, huku ikiendelea kushirikiana na Serikali katika kuboresha huduma za vipimo mkoani Tanga.






Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongoza Ujumbe wa Tanzania kwenye mazungumzo Rasmi na Ujumbe wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) ulioongozwa na Rais wa Nchi hiyo, Mhe. Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo katika Ikulu Ndogo ya Zanzibar, tarehe 18 Agosti, 2026.


 


Top News