Mbunge wa Mbinga Vijijini na Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Judith Salvio Kapinga, akiambatana na Mkuu wa Wilaya ya Mbinga, Mhe. Kisare Makori, pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga, Joseph Kashushura, wamekutana na Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, Septemba 4, 2026, jijini Dodoma, kujadili changamoto zinazotokana na shughuli za uchimbaji wa makaa ya mawe mkoani Ruvuma.

Katika kikao hicho, viongozi hao waliwasilisha kero za wananchi kuhusu ulipaji wa fidia kwa wanaoathiriwa na shughuli za uchimbaji, utekelezaji wa Wajibu wa Kampuni kwa Jamii (CSR), pamoja na baadhi ya kampuni kutotekeleza kwa wakati wajibu mbalimbali unaohusiana na maeneo wanayofanyia shughuli.

Mhe. Kapinga amesema changamoto hizo zimekuwa zikigusa maisha ya wananchi, ikiwemo upatikanaji wa maji, barabara na huduma za afya, hivyo kuomba Wizara ya Madini kuchukua hatua kuhakikisha kampuni zinazofanya shughuli za uchimbaji zinatimiza wajibu wao kwa jamii.

Akijibu hoja hizo, Mhe. Mavunde ameahidi kuwa Wizara yake itashughulikia changamoto hizo ndani ya mwezi mmoja, huku akiiagiza Tume ya Madini kufika mkoani Ruvuma na kukutana na wamiliki wa migodi pamoja na wananchi kwa ajili ya kutafuta suluhu na kuhakikisha changamoto zinazohusiana na shughuli za uchimbaji zinapatiwa ufumbuzi.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Mbinga na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga wameshauri kuwekwa kwa mikakati madhubuti ya kukusanya madeni ya mapato yanayokaribia asilimia 70.







CHAANI, ZANZIBAR


NAIBU Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Ndg. Abdi Mahmoud Abdi, amesema CCM inaandaa mkakati imara wa kuimarisha uhai wa chama hicho ili kiendelee kudumu na kutoa mchango mkubwa kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.

Ndg. Abdi amesema hayo leo, Septemba 5, 2026, wakati akizungumza na viongozi pamoja na wajumbe wa Kamati za Siasa za Mkoa na Wilaya katika Jimbo la Chaani, Zanzibar.

Amepongeza hatua zinazochukuliwa na viongozi wa Jimbo la Chaani katika kuimarisha maendeleo ya chama na wananchi, akisisitiza umuhimu wa kuhakikisha rasilimali za chama zinasimamiwa kwa ufanisi na kutumika kwa manufaa ya chama, wananchi na Taifa.

Amesema moja ya malengo ya ziara yake ni kukagua mali za CCM na kujionea namna zinavyosimamiwa na kuendelezwa ili ziweze kutoa tija kwa chama na wananchi.

Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Chaani, Ndg. Ayoub Mohammed Mahmoud, amesema jimbo hilo lina mali mbalimbali zinazoweza kuchangia maendeleo ya CCM, ikiwemo fremu za maduka pamoja na miradi mingine ya maendeleo inayotekelezwa katika maeneo mbalimbali ya jimbo hilo.

Amesema viongozi wanaendelea na mpango wa ujenzi wa jengo la CCM litakaloendana na hadhi ya chama, huku likiwa na huduma mbalimbali pamoja na ukumbi mkubwa utakaotumika kwa shughuli za chama na shughuli za kijamii.

Hata hivyo, Mbunge huyo ametaja ukosefu wa miundombinu ya barabara za kisasa kuwa miongoni mwa changamoto zinazolikabili Jimbo la Chaani, akisema hali hiyo inarudisha nyuma kasi ya maendeleo katika baadhi ya maeneo.

Akitoa ufafanuzi kuhusu changamoto hizo, Ndg. Abdi amesema amezipokea na atazifanyia kazi kwa lengo la kuhakikisha zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati.

Awali, mara baada ya kuwasili Jimboni Chaani, Ndg. Abdi alipokea taarifa ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za jimbo hilo, ikiwemo miradi ya maendeleo ya chama na jitihada za kuwawezesha wananchi kiuchumi.

Taarifa hiyo pia imeeleza hatua zinazochukuliwa katika kuwawezesha vijana kupata elimu, kuboresha huduma za michezo pamoja na kuhamasisha ushiriki wa wananchi katika shughuli mbalimbali za maendeleo.



















Na Benny Mwaipaja, Kigali-Rwanda

Waziri wa Fedha Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar akiwa na Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Juma Homera, na Viongozi wengine wa Serikali wameshiriki ufunguzi wa mikutano ya Mwaka ya Umoja wa nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika wa Kupambana na Utakasishaji Fedha Haramu na Ufadhili wa Ugaidi (ESAAMLG), uliofanyika leo tarehe 4 Septemba 2026, katika Hoteli ya Serena, Jijini Kigali nchini Rwanda.

Mikutano hiyo inajumuisha Mkutano wa 52 wa Maafisa Waandamizi na Mkutano wa 26 wa Baraza la Mawaziri, pamoja na Mkutano wa 9 wa Majadiliano kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi.

Mikutano hii imewakutanisha viongozi wa Serikali katika ngazi ya Mawaziri na Makatibu Wakuu wa Fedha, Katiba na Sheria, Mambo ya Ndani na maafisa waandamizi kutoka nchi wanachama wa Ukanda wa Mashariki na Kusini mwa Afrika lengo likiwa kuimarisha juhudi za pamoja za kupambana na utakasishaji fedha haramu, ufadhili wa ugaidi, na ufadhili wa silaha za maangamizi.

Kauli mbiu ya mikutano ya mwaka huu inalenga kuweka msukumo wa kutoka kwenye kufuata matakwa ya kiufundi kwenda kwenye kuonesha matokeo halisi katika mifumo ya kupambana na uhalifu wa kifedha ndani ya ukanda wa Mashariki na Kusini mwa Afrika.

Wakizunguza wakati wa ufunguzi wa mkutano huo, viongozi mbalimbali walielezea changamoto ya kuongezeka kwa tishio la utakasishaji fedha haramu, ufadhili wa ugaidi na silaha za maangamizi na kutoa wito kwa nchi wanachama wa ESAAMLG kuweka mikakati ya pamoja ya kukabiliana na changamoto hizo kwa kuongeza uwazi na usalama wa sekta ya fedha.

Ushiriki wa Tanzania katika Mikutano hii utaongeza ushirikiano kati yake na nchi nyingine wanachama katika masuala ya uchunguzi wa miamala shuku, ufuatiliaji wa fedha haramu na ujenzi wa mazingira salama ya biashara na uwekezaji hivyo kukuza imani ya wawekezaji na kuimarisha maendeleo ya uchumi na kijamii.

Mkutano huo unatarajiwa kutoa maazimio na mapendekezo yatakayosaidia nchi wanachama kuimarisha sera, sheria na mifumo ya taasisi zao kwa lengo la kulinda uchumi wa mataifa yao dhidi ya matumizi haramu ya mifumo ya kifedha.

Viongozi wengine kutoka Tanzania walioshiriki ufunguzi huo ni pamoja na Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Dkt. Seif Abdallah Shekalaghe, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango-Zanzibar, Bw. Aboud Hassan Mwinyi, Kamishna wa Kitengo cha FIU, Bw. Majaba Magana, Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania Bi. Sauda Msemo, wakuu wa taasisi, wataalamu wa sekta ya fedha, wasimamizi wa taasisi za kifedha na wadau wengine wa maendeleo kutoka nchi mbalimbali za ukanda huo.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb)(kulia), Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Juma Homera (Mb) (kushoto) na Naibu Gavana na Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki Kuu ya Rwanda, Bw. Nick Barigye, wakiwa katika picha wakati wa hafla ya ufunguzi wa mikutano ya Mwaka ya Umoja wa nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika wa Kupambana na Utakasishaji Fedha Haramu na Ufadhili wa Ugaidi (ESAAMLG), iliyofanyika katika Hoteli ya Serena, Jijini Kigali nchini Rwanda.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb)(kulia), akiteta jambo na na Naibu Gavana na Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki Kuu ya Rwanda, Bw. Nick Barigye (katikati), wakati wa hafla ya ufunguzi wa mikutano ya Mwaka ya Umoja wa nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika wa Kupambana na Utakasishaji Fedha Haramu na Ufadhili wa Ugaidi (ESAAMLG), iliyofanyika katika Hoteli ya Serena, Jijini Kigali nchini Rwanda. Kushoto ni Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Juma Homera (Mb).
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb)(katikati), Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Juma Homera (Mb) (kushoto) na Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bi. Sauda Msemo, wakifuatilia hafla ya ufunguzi wa mikutano ya Mwaka ya Umoja wa nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika wa Kupambana na Utakasishaji Fedha Haramu na Ufadhili wa Ugaidi (ESAAMLG), iliyofanyika katika Hoteli ya Serena, Jijini Kigali nchini Rwanda.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) na Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Juma Homera (Mb), wakiwa katika picha ya pamoja na Mawaziri wengine wa Fedha wanchi wanachama wa Umoja wa nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika wa Kupambana na Utakasishaji Fedha Haramu na Ufadhili wa Ugaidi (ESAAMLG), mara baada ya hafla ya  ufunguzi wa mikutano ya Mwaka ya Umoja huo iliyofanyika katika Hoteli ya Serena, Jijini Kigali nchini Rwanda.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Kigali, Rwanda)






-Mpango wa dampo la Pugu kushirikisha sekta binafsi waiva… madiwani watoa msimamo


Na Said Mwishehe,Michuzi TV


BARAZA la Madiwani la Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam limekutana katika kikao maalum kilichokuwa na lengo la kutekeleza maagizo ya Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kuhusu kutafuta ufumbuzi wa changamoto ya uchafu katika Jiji hilo.

Katika kutekeleza maagizo hayo pamoja na mambo mengine kikao hicho kilichoongozwa na Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam Nurdin Bilal maarufu Shetta pamoja na Katibu wa kikao hicho ambaye ni Mkurugenzi wa Jiji hilo Elihuruma Mabelya wamekubaliana kushirikisha sekta binafsi kupitia mpango wa PPP kuendesha dampo la Pugu kinyamwezi ambalo kwa sasa limezidiwa.

Katika kikao hicho maalum kilichofanyika leo Septemba 4,2026 Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam Elihuruma Mabelya amewasilisha mpango wa kushirikiaha sekta binafsi kusimamia dampo la Pugu Kinyamwezi ambalo ndilo linatumika kutupwa taka zote zinazozalishwa katika Jiji hilo.

“Kumekuwa na mpango mkakati wa Jiji la Dar es salaam unaotaka asilimia 80 ya taka zipelekwe dampo la Pugu na ukweli mpango huo umefeli.Kutokana na ongezeko la watu katika Jiji la Dar es Salaam umefika wakati wa kushirikisha sekta binafsi kupitia PPP ili kupata suluhu ya kudumu.”

Akifafanua zaidi katika kikao hicho Mabelya amesema maagizo yaliyotolewa na Rais Dk.Samia Suluhu Hassan yanapaswa kutekelezwa kwa haraka na jambo muhimu zaidi kuwa na suluhu ya kudumu.

“Tumepokea maagizo ya Rais Samia lakini pia Spika wa Bunge ameonesha kutoridhishwa n hali ya usafi katika Jiji la Dar es Salaam.Tumewasikia viongozi wetu na tumechukua hatua mbalimbali na leo tumekutana katika kikao maalum kujadili maagizo tuliyopewa.”

Kuhusu taka zinazozalishwa katika Jiji la Dar es Salaam amesema kwa siku zinazalishwa kiasi cha taka tani 1320 kwa siku na zinazopelekwa dampo la Pugu ni tani 792 pekee wakati taka zinaozalishwa katika halmashauri zote ni kati ya tani 2500 hadi 3000 kwa siku.”Taka nyingi bado zipo mtaani na zinaathiri wanannchi kiafya na mazingira.”

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Ilala Edward Mpogolo amepongeza kufanyika kikao hicho kutekeleza maagizo ya Rais na kusisitiza Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam linamshukuru Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kwa kusema ukweli kuhusu hali ya usafi katika Jiji hilo.

“Ni heshima kubwa kwa Kiongozi akishatoa maagizo kuona maagizo yanatekelezwa.Niwapongeze Baraza l madiwani kwa kikao hichi kilichokutana kutekeleza maagizo tuliyopewa.”

Pamoja na hayo amesema changamoto ya dampo la Pugu halmashauri imekuwa inatumia nguvu nyingi katika dampo hilo na mashine za kushusha taka zimekufa.

“Mtu anayekwambia ukweli anakupenda,hali ni mbaya.Heka 400 kabla ya kuingia dampo taka kila mahali na kwa miaka minne kumekuwa na siasa nyingi kuhusu dampo hilo..Nawapongeza kwa kutekeleza agizo la Rais Samia Suluhu Hassan.

“Spika amesema bungeni wapi ambapo wakandarasi wanakwamisha.Tunajua mpango huu mzuri wa kushirikisha sekta binafsi katika dampo letu kuna watu watanuna kwa maslahi yao binafsi. Hivyo kazi ambayo imebakia ni watalaam kukaa na kuona jinsi mikataba itakavyokuwa kwani kuingia PPP kuna mikataba ya kisheria .
“Rais amezungumza miaka yote tunakwenda tunarudi nyuma jambo halifiki mwisho kama tumekanyaga mdudu.Sasa twendeni tukatekeleze mpango huu wa dampo na dira ya 2050 inaeleza umuhimu wa kushirikisha sekta binafsi katika kutekeleza mipango ya Serikali.”










Jumla ya wananchi 3,879 wamenufaika na Kambi Maalum ya Matibabu na Upasuaji wa Macho iliyoendeshwa na Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Qatar Charity, iliyohitimishwa leo Septemba 4, 2026 katika viwanja vya Kituo cha Afya Sebuleni, Mkoa wa Mjini Magharibi.


Akizungumza wakati wa hafla ya kuhitimisha kambi hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi, Mhe. Mohammed Ali Abdalla, amesema huduma hiyo imeleta mapinduzi makubwa katika upatikanaji wa matibabu ya macho Zanzibar kwa kuwafikia wananchi moja kwa moja katika maeneo yao na kueleza kuwa serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuthamini ushirikiano na Muhimbili na Qatar Charity katika kuimarisha huduma za afya kwa wananchi.
“Leo tunashuhudia maelfu ya wananchi wakirejeshewa matumaini ya kuona. Ushirikiano huu umeonesha kuwa tukifanya kazi pamoja tunaweza kusogeza huduma za kibingwa karibu na wananchi na kupunguza adha ya kusafiri kutafuta matibabu." amesema Mhe. Abdalla

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dkt. Delilah Kimambo, amesema mafanikio ya kambi hiyo yanadhihirisha dhamira ya Muhimbili ya kuwafikishia Watanzania huduma za kibingwa popote zilipo hitajika, huku akiwapongeza madaktari na watumishi wote walioshiriki kufanikisha zoezi hilo.

“Muhimbili itaendelea kuwa mshirika wa karibu wa Zanzibar katika kuimarisha huduma za afya. Furaha yetu kubwa ni kuona mamia ya wagonjwa wakirejea nyumbani wakiwa wamepata tena uwezo wa kuona na kuanza maisha mapya.” ameeleza Dkt. Kimambo

Kambi hiyo ilianza Agosti 29 hadi 31, 2026 katika Kituo cha Afya Kinduni, Mkoa wa Kaskazini Unguja, ambapo wananchi 971 walifanyiwa uchunguzi na kupatiwa matibabu ya magonjwa mbalimbali ya macho, huku 136 wakifanyiwa upasuaji wa mtoto wa jicho. Kutokana na mwitikio mkubwa wa wananchi, huduma zilihamishiwa Kituo cha Afya Sebuleni kuanzia Septemba 1 hadi 4, 2026, ambako wagonjwa 2,769 walihudumiwa na 237 kufanyiwa upasuaji.

Kwa kipindi chote cha siku saba, jumla ya wananchi 6880 wameonwa, 3,879 wamepata huduma za uchunguzi na matibabu ya macho, 378 wamefanyiwa upasuaji wa mtoto wa jicho kwa njia ya tundu dogo na 406 walipatiwa miwani bila malipo. Upasuaji huo ulifanyika kwa kutumia gari maalum la upasuaji, ikiwa ni mara ya kwanza nchini Tanzania huduma hiyo kutolewa kwa mfumo huo wa kisasa.






 

Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) na Kampuni ya Van Mo zimesaini Hati ya Makubaliano (MoU) yenye lengo la kuimarisha ushirikiano katika kuendeleza ujuzi kwa vijana na kuwaandaa kupata ajira kulingana na mahitaji ya soko.

Hati hiyo imesainiwa leo, Septemba 4, 2026, jijini Dodoma na Mkurugenzi Mkuu wa VETA, CPA Anthony Kasore, pamoja na Meneja Mkuu wa Kampuni ya Van Mo, Fathi Ahmed.

Ushirikiano huo unalenga kuhakikisha mafunzo ya ufundi stadi yanaendana na mahitaji ya sekta ya viwanda na biashara, huku wahitimu wakijengewa umahiri, ubunifu, tija, maadili na uelewa wa usalama kazini, Van Mo pia itatoa fursa za mafunzo kwa vitendo na ajira kwa wahitimu wenye sifa zinazokidhi mahitaji yake.

Maeneo yatakayohusika katika makubaliano hayo ni pamoja na udereva wa magari makubwa, usimamizi wa vyombo vya usafiri, uchukuzi na uhifadhi wa mizigo, usimamizi wa mnyororo wa ugavi, ukaguzi na ukarabati wa magari pamoja na mifumo ya umeme na elektroniki ya magari.

Maeneo mengine ni uendeshaji wa maghala na usimamizi wa stoo, uendeshaji wa vituo vya mafuta, ujenzi na usimamizi wa majengo na miundombinu, shughuli za utalii na ukarimu, pamoja na kilimo na uhifadhi wa mazao.

Katika mashauriano ya awali yaliyofanyika Agosti 31, 2026, Mkuu wa Uzingatiaji wa Sheria, Kanuni na Taratibu wa Van Mo, Hamis Lugusha, alisema kampuni hiyo ina mahitaji makubwa ya madereva kutokana na ongezeko la magari, akieleza kuwa mwaka huu imepokea magari mapya 100 yanayohitaji madereva, huku magari mengine 150 yakitarajiwa kuongezwa mwakani.

Lugusha alisema pamoja na mahitaji hayo, kampuni imekuwa ikipata changamoto ya kupata madereva wanaokidhi viwango vinavyohitajika, hasa katika uadilifu, uaminifu, uwajibikaji na utamaduni wa kazi, hali hiyo imeifanya kampuni kuona umuhimu wa kushirikiana na VETA katika kuwaandaa madereva kuanzia misingi ya taaluma na maadili.

Kwa upande wake, CPA Kasore alisema programu hiyo inaweza kuwahusisha waombaji wenye mafunzo na wasio na mafunzo ya udereva, huku wenye uzoefu wakitakiwa kuchujwa kwa kuzingatia historia ya utendaji wao, alisema hatua hiyo itasaidia kupata waombaji ambao uzoefu wao unaendana na tabia na viwango vinavyohitajika na mwajiri.

Naye Mkurugenzi wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Dkt. Abdallah Ngodu, alipendekeza ushirikiano huo utekelezwe kupitia mfumo wa uanagenzi, utakaowezesha Van Mo kushiriki katika kuwajenga wanafunzi kupitia mazingira halisi ya kazi, pamoja na kuwapa misingi ya nidhamu, uwajibikaji na utamaduni unaohitajika katika sekta ya usafirishaji.

Katika utekelezaji wa hati hiyo, VETA itatoa au kuwezesha programu za mafunzo, kushiriki katika uandaaji na mapitio ya mitaala, tathmini na utoaji wa vyeti vya umahiri, wakati Van Mo itatoa taarifa kuhusu mahitaji ya ujuzi, fursa za mafunzo kazini, mrejesho wa utendaji wa wanafunzi na wahitimu, pamoja na ajira kwa watakaokidhi vigezo vya kampuni.












Top News