Na Victor Masangu,Kibiti

Mwenyekiti wa Jumuiya ya wazazi Taifa Ndg. Fadhili Maganya ameridhishwa na utekelezaji wa mradi wa maji ambao unatakelezwa na Wakala wa maji na usafi wa mazingira vijijini (RUWASA) Wilaya ya Kibiti ambapo amesema kwamba mradi huo ni mkombozi mkubwa katika kuwahudumia kwa kiasi kikubwa wananchi hao upatikanaji wa maji safi na salama ambapo itawapunguzia adha wanannchi hao kutembea umbari mrefu.

Hayo ameyabainishwa wakati wa ziara yake ya kikazi katika Wilaya ya Kibiti yenye lengo la kuweza kuimarisha chama, kuangalia utekelezaji wa Ilani pamoja na jumuiya zake zote sambamba na kutembelea na kukagua miradi mbali mbali ya maendeleo, ikiwemo sekta ya elimu pamoja na sekta ya maji.

Mwenyekiti huyo amesisitiza kwa uongozi wa Ruwasa kuendelea kuhakikisha wanaweka ulinzi wa kutosha katika mradi huo ambapo amesema chanzo hicho ni muhimu sana kwani ndio tegemezi kubwa la wananchi wa Wilaya ya Kibiti katika suala zima la upatikanaji wa maji safi na salama na kuwahimiza kutunza chanzo cha maji hayo pamoja miundombinu iliyopo.

"Nipende kuchukua nafasi hii kuwapongeza kwa dhati uongozi mzima wa Ruwasa kwa kutekeleza mradi huo wa maji ambao utakuwa ni msaada mkubwa kwa wananchi wa Wilaya ya Kibiti,"amebainisha Mwenyekiti.

Akizungumza katika mkutano wa ndani na wanachama wa chama hicho amewaomba viongozi kuhakikisha kwamba wanatekeleza ilani ya chama kwa vitendo ikiwemo suala la kusimamia fursa za mikopo ya asilimia 10 ambayo inatolewa na Halmashauri.

Pia amewaagiza viongozi wa chama pamoja na madiwani kuhakikisha wanasimamia fedha zinazotolewa kwa ajili ya miradi ya maendeleo.

Meneja huyo amebainisha kwamba lengo kubwa la ukarabati wa mradi huo ni kwa ajili ya kuweza kutatua changamoto ya maji ambazo zinawakabiliwa wananchi wa Wilaya ya Kibiti na kuunga juhudi za serikali ya awamu ya sita katika kuhakikisha ina mtua mama ndoo kichwani

Amebainisha ukarabati wa.mradi wa maji Kibiti mjini umetekelezwa kwa kiasi cha zaidi ya shilingi milioni 312 ambazo fedha hizo zimetolewa na serikali kuu kupitia mfuko wa maji wa fedha Kitaifa (NWF) na kwamba utakuwa ni mkombozi mkubwa katika kutatua changamoto hizo zilizokuwa zinawakabili wananchi.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kibiti Kanali Joseph Kolombo amempongeza kwa dhati Mwenyekiti wa wazazi Taifa kwa kutekeleza ilani ys chama kwa vitendo ikiwemo suala la kufanya ziara ya kikazi ambayo imekuwa na mafanikio makubwa kutokana na kuweza kukutana na viongozi wa serikali, taasisi wezeshi pamoja na chama.

Kanali Kolombo amebainisha kwamba hali ya amani na utulivu katika Wilaya ya Kibiti inaendelea vizuri na kwamba katika utekelezaji wa ilani wameweza kupokea kiasi cha shilingi milioni 528 kwa ajili ya ujenzi wa shule ya Mchukwi ambapo pia wamepokeai kisi cghha shilingi milioni 700 kwa lengo la kuboresha miundombinu ya barabara hususan zinazowenda maeneo ya Delta na sehemu nyingine.

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Taifa ameendelea na ziara yake ya kikazi katika Wilaya ya Kibiti ambapo ameweza kupata fursa ya kuzungumza na wanachama wa CCM, viongozi wa serikali,taasisi wezeshi pamoja na kutembelea baadhi ya miradi mbali mbali ya maendeleo katika sekta ya maji pamoja na elimu.





Mrajis Msaidizi wa Vyama vya Ushirika Mkoa wa Dodoma, Joseph Chitinka, amewataka wakazi wa Dodoma, mikoa jirani na Tanzania kwa ujumla kujitokeza kwa wingi kushiriki maonesho ya kilimo Nanenane yanayoendelea katika viwanja vya Nanenane jijini Dodoma na kutembelea Banda la Kijiji cha Ushirika.

Chitinka amesema Banda hilo limeandaliwa kwa mara ya tatu mfululizo na Tume ya Maendeleo ya Ushirika kwa kushirikiana na Shirikisho la Vyama vya Ushirika TFC kwa lengo la kuonesha bidhaa, shughuli mbalimbali pamoja na huduma zinazotolewa na vyama vya ushirika nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari Agosti 1, 2026 katika viwanja vya Nanenane jijini Dodoma, amesema Banda la Kijiji cha Ushirika ni jukwaa maalum linalowakutanisha wadau wa sekta hiyo na kutoa fursa kwa wananchi kufahamu mchango wa vyama vya ushirika katika maendeleo ya kiuchumi.

Amesema kupitia Banda la Mkoa wa Dodoma linaloratibiwa na Chama Kikuu cha Ushirika Mkoa wa Dodoma (DORECU), wananchi wataweza kuona mazao 12 yanayooneshwa, yakiwemo ufuta, choroko na mbaazi.

Aidha, amesema wananchi watapata elimu kuhusu taratibu na sifa za kujiunga na vyama vya ushirika, hususan vya mazao, pamoja na fursa za mikopo zinazopatikana kupitia ushirika.

“Maonesho haya yatasaidia wananchi kufahamu namna vyama vya ushirika vinavyomuinua mkulima, kuongeza kipato na kumsaidia mwananchi kujikwamua kiuchumi,” amesema Chitinka.

Ameongeza kuwa Mkoa wa Dodoma unajivunia mchango wa sekta ya ushirika katika kuchochea maendeleo ya wananchi, huku ukiendelea kusimamia kauli mbiu ya “Linda Ushirika, Chagua Uadilifu.”




Taasisi ya Kuthibiti Ubora wa Mbegu Tanzania (TOSCI) imewataka wakulima nchini kutonunua mbegu yoyote ambayo haina lebo ya utambuzi ya TOSCI, ikieleza kuwa lebo hiyo ndiyo uthibitisho kuwa mbegu imekaguliwa na kuthibitishwa ubora wake.

Wito huo umetolewa na Mkurugenzi Mkuu wa TOSCI, Nyasebwa E. Chimagu, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya Kilimo ya Nanenane yanayofanyika jijini Dodoma Agosti 1, 2026.

Chimagu alisema matumizi ya mbegu bora ni msingi wa kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao na kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, amesema kuwa wakulima wanapaswa kuhakikisha mbegu wanazonunua zimefungashwa katika vifungashio rasmi vyenye lebo ya TOSCI.

Alieleza kuwa wakulima wanaweza kuhakiki uhalali wa lebo hiyo kwa kutumia simu za mkononi ili kubaini kama mbegu ni halisi au la, hatua ambayo itawasaidia kuepuka kununua mbegu bandia zinazoweza kusababisha hasara.

Aidha, alisema TOSCI inaendelea kutoa elimu kupitia mabanda yake katika Maonesho ya Kilimo ya Nanenane kuhusu umuhimu wa kutumia mbegu zilizothibitishwa, pamoja na kutoa mafunzo kwa wazalishaji na wafanyabiashara wa mbegu kuhusu taratibu za uzalishaji, usafirishaji na biashara ya mbegu.

Chimagu alibainisha kuwa matumizi ya mbegu bora, sambamba na kuzingatia kanuni bora za kilimo, yanaweza kumwezesha mkulima kuvuna kati ya tani tano hadi kumi kwa hekta.

Aliwahimiza wakulima kutumia Maonesho ya Kilimo ya Nanenane kama fursa ya kupata elimu kuhusu mbegu bora na teknolojia mbalimbali za kilimo zitakazowaongezea tija katika msimu wa kilimo wa mwaka 2026/2027.


Wakala wa Mbegu za Kilimo (ASA) umetangaza mpango wa kuongeza uzalishaji wa mbegu bora hadi kufikia tani 15,000 baada ya mavuno yanayotarajiwa hivi karibuni, hatua inayolenga kuongeza upatikanaji wa mbegu bora kwa wakulima nchini.

Mtendaji Mkuu wa ASA, Mhandisi Innocent C. Masaka , ameyasema hayo Leo Agosti 1, 2026, wakati akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya Kilimo ya Nanenane jijini Dodoma ambapo  hadi sasa wakala huo umezalisha tani 7,000 za mbegu, huku ukiendelea kuimarisha uzalishaji kupitia mashamba yake yaliyopo katika kanda mbalimbali za nchi na mahitaji ni kufikia Tani elfu 27.

Amesema ASA katika kuhakikisha wanaongeza uzalishaji wambegu wamejipanga kupanua ushirikiano na sekta binafsi kwa kuwapatia teknolojia za uzalishaji wa mbegu bora ili kuongeza kiwango cha uzalishaji na kuhakikisha wakulima wengi zaidi wanapata mbegu zenye ubora unaohitajika kwa wakati.

Mhandisi Masaka amesema mbegu zinazozalishwa na ASA zimeendelea kuonesha matokeo mazuri katika kanda zote za kilimo nchini, zikiwemo kusini, kaskazini, mashariki na magharibi, huku zikiwa na uwezo wa kuhimili ukame unaotokana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Aidha, amewahimiza wakulima kutumia mbegu bora zilizothibitishwa na TOSCI ili kuongeza tija ya uzalishaji, amesema ASA imeendelea kuimarisha mfumo wa usambazaji kupitia mawakala, wasambazaji wakubwa na Wakala wa Huduma za Ugani Tanzania (NAESA), ambao huwafikishia wakulima teknolojia na mbegu bora kwa wakati.

Amewaalika wananchi kutembelea banda la ASA katika Maonesho ya Nanenane ili kujifunza kuhusu teknolojia za uzalishaji wa mbegu bora na huduma mbalimbali zinazotolewa na wakala huo kabla ya maonesho hayo kuhitimishwa Agosti 8, 2026.







 

Na.Mwandishi wetu

Kampuni ya Mbolea Tanzania (TFC) imeanza utekelezaji wa mpango mkubwa wa kuongeza upatikanaji wa mbolea nchini kwa kuagiza tani 200,000 za mbolea kwa msimu wa kilimo wa mwaka huu, sambamba na uwekezaji katika viwanda vya kuchanganya mbolea na uchakataji wa chokaa ili kuongeza tija ya uzalishaji wa mazao.

Mkurugenzi Mkuu wa TFC, Samuel Ahadi Mshote, amesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha wakulima wanapata mbolea bora kwa wakati, kuongeza matumizi ya pembejeo na kuimarisha usalama wa chakula pamoja na uchumi wa kilimo nchini.

Akizungumza leo Agosti 1,2026 kwenye Maonesho ya 49 ya Kilimo ya Nane Nane yanayoendelea kitaifa katika viwanja vya Dkt.John Samuel Malecela jijini Dodoma, Mshote amesema TFC ina jukumu la kuhakikisha upatikanaji wa mbolea zenye ubora unaokidhi mahitaji ya wakulima, huku ikijiandaa kuanza uzalishaji wa mbolea zinazochanganywa kulingana na afya ya udongo na mahitaji ya mazao mbalimbali.

Amesema katika awamu ya kwanza kampuni imeagiza tani 70,000 za mbolea, ambapo tani 35,000 za mbolea aina ya DAP tayari zimewasili nchini na zinafungashwa katika Bandari ya Dar es Salaam kwa ajili ya kusambazwa kwa wakulima kupitia utaratibu wa pembejeo zenye ruzuku ya Serikali.

Aidha, amesema tani nyingine 40,000 za mbolea aina ya Urea zinatarajiwa kuwasili ndani ya muda mfupi ili kuendelea kukidhi mahitaji ya msimu wa kilimo unaoanza.

"Tunataka kuhakikisha hakuna mkulima anayekosa mbolea kwa sababu ya upungufu wa usambazaji. Ndiyo maana tumejipanga kuongeza uagizaji na kuimarisha mtandao wa usambazaji nchini kote," amesema  Mshote.

Amesema TFC imepanua mtandao wake wa huduma kwa kuongeza vituo vya mauzo kutoka nane hadi 26 vilivyopo katika mikoa 22 ya Tanzania Bara, hatua iliyorahisisha wakulima kupata mbolea karibu na maeneo yao.

Mbali na vituo hivyo, kampuni hiyo inashirikiana na zaidi ya mawakala 600 wa pembejeo za kilimo, vyama vya ushirika 29 (AMCOS) pamoja na halmashauri mbalimbali ili kuhakikisha mbolea zinawafikia wakulima hadi ngazi ya vijiji.

Kwa mujibu wa Mshote, tangu TFC ilipoanza kusambaza mbolea mwaka 2022, tayari zaidi ya tani 350,000 za mbolea za ruzuku zimesambazwa kwa wakulima wanaojihusisha na uzalishaji wa mpunga, mahindi, mboga mboga, vitunguu na mazao mengine ya biashara.

Katika hatua nyingine, amesema kampuni hiyo inakamilisha ufungaji wa mtambo wa kisasa wa kuchanganya mbolea katika jiji la Dar es Salaam, ambao utakuwa na uwezo wa kuzalisha tani 300,000 za mbolea kwa mwaka kulingana na mahitaji ya udongo na mazao husika.

Amesema uwekezaji huo utapunguza utegemezi wa uagizaji wa mbolea kutoka nje ya nchi na kuongeza upatikanaji wa mbolea maalumu kwa mazao ya kimkakati kama vitunguu, ufuta, parachichi na mazao mengine yenye thamani kubwa kiuchumi.

Sambamba na hilo,amesema  TFC imeanza kutekeleza mradi wa uchimbaji na uchakataji wa chokaa mkoani Tanga baada ya kupatiwa eneo na Halmashauri ya Jiji la Tanga. Chokaa hicho kitatumika kurekebisha tindikali kwenye udongo pamoja na kuwa malighafi muhimu katika uzalishaji wa mbolea.

Mshote amesema mafanikio ya utekelezaji wa mpango wa ruzuku ya mbolea yameongeza matumizi ya pembejeo nchini kutoka tani 300,000 hadi zaidi ya tani milioni 1.2 kwa mwaka, huku takribani asilimia 80 ya wanufaika wakiwa ni wakulima wadogo.

Amesema ongezeko hilo limechangia kuimarika kwa uzalishaji wa mazao na kuiwezesha Tanzania kufikia kiwango cha zaidi ya asilimia 130 cha kujitosheleza kwa chakula.

Aidha, matumizi ya mbolea kwa hekta yameongezeka kutoka kilo 16 hadi kilo 24, huku Serikali na wadau wa sekta hiyo wakilenga kufikia kiwango cha kilo 30 kwa hekta kama kinavyoelekezwa na Azimio la Abuja kuhusu matumizi ya mbolea barani Afrika.

Amesema utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 unahitaji ushirikiano wa karibu kati ya Serikali, sekta binafsi, taasisi za umma na wananchi ili kuhakikisha malengo yaliyowekwa yanafikiwa kwa wakati na kwa ufanisi.

Ameeleza kuwa dhamira ya Serikali ni kuona Tanzania inafikia uchumi shindani, wenye tija na jumuishi ifikapo mwaka 2050, huku akiahidi kuwa wataendelea kusimamia kwa dhati utekelezaji wa mipango na vipaumbele vilivyowekwa ili kuhakikisha maono hayo yanageuka kuwa matokeo yanayoonekana kwa manufaa ya Watanzania wote.

Mshote amewataka wakulima kutembelea banda la TFC katika Maonesho ya Nane Nane ili kupata elimu kuhusu matumizi sahihi ya mbolea na kufahamu aina zinazofaa kwa mazao na mazingira yao, akisisitiza kuwa matumizi ya pembejeo bora ndiyo msingi wa kuongeza tija, kipato cha mkulima na ukuaji wa sekta ya kilimo nchini.




Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), akizungumza na wadau wakati wa Wiki ya Tisa ya Viwanda ya SADC (SADC Industrialisation Week 2026), inayoadhimishwa katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (ICC), jijini Durban, Afrika Kusini. Mkutano huo unawakutanisha viongozi wa serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo kujadili mikakati ya kuharakisha maendeleo ya viwanda na biashara ya kikanda.

DURBAN - AFRIKA KUSINI

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), Bi. Khadija Ngasongwa, amezishauri nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kuwekeza zaidi katika maendeleo ya viwanda na miundombinu ili kuwawezesha wanawake na vijana kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji.

Bi. Ngasongwa ametoa wito huo jijini Durban, Afrika Kusini, wakati akishiriki Mkutano wa Wiki ya Tisa ya Viwanda ya SADC unaoendelea nchini humo.

"Ushiriki wa FCC katika wiki hii unalenga kuhakikisha sera na miongozo ya ushindani wa haki inazingatiwa katika maendeleo ya viwanda. Tunataka kuona viwanda vya ukanda wetu vinakuwa na ushindani, vinatoa fursa kwa wanawake na vijana, na vinatoa bidhaa zenye ubora kwa walaji," alisema Bi. Ngasongwa.

Ameongeza kuwa uwekezaji katika viwanda vya kuongeza thamani ya malighafi utasaidia kuwainua kiuchumi wanawake na vijana, kupanua masoko ya bidhaa za nchi za SADC na kuongeza mapato ya fedha za kigeni.

Akizungumzia ushiriki wa Tanzania, Bi. Ngasongwa amesema mkutano huo unaendana na vipaumbele vya maendeleo ya Tanzania hususan katika sekta za madini, kilimo, bidhaa za afya, miundombinu na ubunifu.

"Ushiriki wa Tanzania una umuhimu mkubwa kwa sababu unajikita katika kuimarisha mnyororo wa thamani. Ni maeneo muhimu katika safari ya Tanzania kuelekea uchumi wa viwanda na kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050," alisema.

Bi. Ngasongwa pia amewataka wadau wa fedha waliopo katika mkutano huo ikiwemo TIB, Exim Bank, BADEA na Nedbank kushirikiana katika kuhamasisha upatikanaji wa mitaji kwa ajili ya miradi ya maendeleo na uwekezaji nchini.

Amehitimisha kwa kusema kuwa Tanzania imebarikiwa kuwa na madini ya kimkakati na rasilimali nyingine. Hivyo ni muhimu kuyachakata ndani ya nchi badala ya kuuza malighafi ili kuongeza thamani, kuzalisha ajira na kuchochea ukuaji wa viwanda.

Mkutano wa Wiki ya Viwanda ya SADC ulifunguliwa rasmi Julai 27, 2026 na ulihitimishwa Julai 31, 2026 na umetoka na maazimio ya kuimarisha ushirikiano wa kikanda katika biashara, uwekezaji na maendeleo ya viwanda kama sehemu ya maandalizi ya Mkutano wa 46 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa SADC utakaofanyika tarehe 17 Agosti, 2026 Jijini Durban, Afrika Kusini.





Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), akizungumza na wadau wakati wa Wiki ya Tisa ya Viwanda ya SADC (SADC Industrialisation Week 2026), inayoadhimishwa katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (ICC), jijini Durban, Afrika Kusini. Mkutano huo unawakutanisha viongozi wa serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo kujadili mikakati ya kuharakisha maendeleo ya viwanda na biashara ya kikanda.



Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), Bi. Khadija Ngasongwa (katikati), akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya washiriki kutoka Tanzania wakati wa Mkutano wa 9 wa Wiki ya Viwanda wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC Industrialisation Week), unaofanyika jijini Durban, Afrika Kusini.



Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Mahusiano kwa Umma, Bi. Roberta Feruzi akitoa maelezo kuhusu huduma zinazotolewa na FCC kwa baadhi ya wadau waliotembelea Banda la Tanzania, pembezoni mwa Mkutano wa Wiki ya Viwanda ya SADC (SADC Industrialisation Week 2026) unaofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (ICC), jijini Durban, Afrika Kusini.

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba ameipongeza Benki ya NMB kwa kuendelea kusogeza huduma za kifedha karibu na wananchi kupitia matumizi ya teknolojia na mkakati wa Rural Banking, akisema Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya biashara na kupunguza gharama za miamala ya kifedha.

Akimkaribisha Waziri Mkuu katika banda la NMB kwenye Maonesho ya Nanenane, Mkuu wa Idara ya Biashara za Serikali wa benki hiyo, Bi. Vicky Bishubo, alisema NMB imeendelea kuwekeza katika sekta ya kilimo, uvuvi na ufugaji, ikiwa tayari imetoa mikopo yenye thamani ya Sh. trilioni 2.3 kwa sekta hizo.

Alisema benki hiyo pia imewawezesha vijana kupata mikopo ya hadi Sh. milioni mbili kupitia teknolojia bila dhamana wala kwenda tawi, huku huduma za Rural Banking zikiendelea kufika katika masoko na minada ya biashara na mifugo katika maeneo mbalimbali nchini.

Mbali na huduma za kifedha, NMB inaendelea kutoa elimu ya fedha kupitia NMB Kijiji Day na kushirikiana na vyuo vikuu kuwajengea vijana ujuzi unaohitajika katika uchumi unaotegemea teknolojia na ubunifu.

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba (kushoto) akisikiliza maelezo kutoka kwa Mkuu wa Idara ya Biashara za Serikali wa Benki ya NMB, Bi. Vicky Bishubo, alipotembelea banda la benki hiyo katika Maonesho ya Kitaifa ya Kilimo Nanenane yanayoendelea kwenye Viwanja vya John S. Malecela, Nzuguni mkoani Dodoma jana. NMB ni mdhamini wa maonesho hayo.







WAZIRI Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba ametoa wito kwa wazalishiaji mbalimbali nchini waboreshe bidhaa zao ili zimudu ushindani wa kimataifa na ziweze kushindana kila siku na siyo wakati wa maonesho tu.

“Bidhaa ambazo tuko nazo zisiwe kwa ajili ya maonesho, bali ndiyo iwe standard ya bidhaa zetu katika maisha yetu. Tukishafikia hatua hiyo, tutakuwa tumetatua mambo mengi kwa mpigo ikiwemo kujihakikishia kwamba bidhaa zetu zinapata soko, ni lazima tuendelee kuoanisha uzalishaji na vigezo vya kimataifa vya masoko,” amesema.

Waziri Mkuu amesema hayo leo (Jumamosi, Agosti Mosi, 2026) wakati akizungumza na mamia ya wananchi waliohudhuria ufunguzi wa Maonesho ya 33 ya Kitaifa ya Wakulima (Nanenane), yaliyofunguliwa rasmi katika Viwanja vya Dkt. John John S. Malecela, Nzuguni, jijini Dodoma.

Amesema kufanya hivyo kutawezesha bidhaa zinazozalishwa kupata masoko popote duniani kutokana na ubora utakaokuwa nazo. “Tutengeneze bidhaa zetu za kila siku kama vile za kwenda kwenye maonesho. Katika maeneo mengi, tatizo siyo soko bali ni viwango vinavyoweza kumsukuma mnunuzi kutamani kununua bidhaa husika. Tukiboresha viwango, bidhaa zitanunuliwa na kwa njia hiyo tutaongeza uzalishaji na hivyo kupata masoko na kuongeza uchumi wa mtu mmoja moja,” amesititiza.

Akielezea kuhusu utoshelevu wa chakula nchini, Waziri Mkuu amesema kuwa nchi ina utoshelevu kwa asilimia 130 na imeongeza mauzo nje ya nchi kwa asilimia 77 na kuwa moja ya chanzo cha uhakika cha fedha za kigeni.

“Haya ni mabadiliko yanayochangiwa na hatua za serikali ya awamu ya sita kwa kuweka mazingira wezeshi na uwekezaji wenye tija kwenye mnyororo mzima wa sekta ya kilimo. Tangu Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, alipoingia madarakani, wakulima wamewezeshwa ruzuku ya pembejeo za kilimo ikiwemo mbolea, zaidi ya tani 700,000 yenye thamani ya zaidi ya shilingi trilioni 1.4,” amesema.

Awali, Waziri Mkuu alitembelea mabanda mbalimbali ya maonesho na kupata maelezo kutoka kwa wajasiriamali wanaoshiriki maonesho hayo ambapo aliipongeza Benki ya NMB kwa kuendelea kuboresha huduma za kifedha na kuzisogeza karibu na wananchi hasa wakazi wa vijijini, vijana na wanawake.

Amesema amefurahishwa na jitihada za benki hiyo za kuwafikia wananchi kupitia huduma za kibenki zinazotolewa kwa kutumia magari maalumu pamoja na kuwafuata wafanyabiashara katika masoko na minada mbalimbali nchini.

“Hatua hizi zinaendana na kiu ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kutaka kuona Watanzania wengi wanapata huduma za uchumi jumuishi wa kifedha (financial inclusion) na hii itasaidia nchi kuondoka kwenye cash economy, itafanya tufike mahali mtu popote alipo ana fedha yake, na hata akitaka mahitaji fedha anayo,” amesema.

Alisema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan itaendelea kuboresha mazingira ya sekta ya fedha, ikiwemo kupunguza gharama za miamala ya kifedha ili kuhakikisha Watanzania wengi zaidi wanapata huduma bora za kibenki na kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji na maendeleo ya uchumi.

Akitoa maelezo mbele ya Waziri Mkuu, Mkuu wa Idara ya Huduma za Serikali wa Benki ya NMB, Bibi Vicky Bishubo, alisema benki hiyo imeendelea kuimarisha upatikanaji wa huduma za kifedha kupitia mpango wa huduma za benki vijijini unaotumia magari maalumu ya huduma za kibenki (mobile branch operations) yanayofika katika vijiji mbalimbali nchini kutoa huduma za kifedha, elimu ya fedha pamoja na mikopo kwa wananchi hususan wanawake na vijana wajasiriamali.

Bibi Bishubo alisema pia Benki ya NMB inaendelea kushirikiana na Serikali kupitia Wizara yenye dhamana ya masuala ya vijana katika utekelezaji wa mpango wa mikopo wa sh. bilioni 200 ulioanzishwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa lengo la kuwawezesha vijana kiuchumi. Alisema benki hiyo imeweka mazingira rafiki na kupunguza vikwazo vinavyoweza kuwazuia vijana kunufaika na mikopo hiyo.

Aidha, alisema benki hiyo inaendelea kushirikiana na taasisi mbalimbali za elimu ya juu, ikiwemo Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Chuo Kikuu cha Dodoma kuandaa programu na mitaala inayolenga kuwaandaa vijana katika matumizi ya huduma za fedha za kidijitali na kuongeza uelewa wao kuhusu sekta ya fedha.

Maonesho hayo ya 33 ya Nanenane yenye hadhi ya Kitaifa na Kimataifa, yanaendeshwa kwa lengo la kukuza uchumi, kuongeza matumizi ya teknolojia bora na kuimarisha ushirikiano wa kimataifa.
WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, amelielekeza Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO) kuendelea kusonga mbele katika kutekeleza dhamira ya Serikali ya kubadilisha sekta ya Uvuvi nchini kuwa ya kibiashara, akisisitiza kuwa uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali umeweka msingi imara wa kuiwezesha Tanzania kunufaika zaidi na rasilimali za uvuvi wa bahari kuu.

Waziri Mkuu ametoa maelekezo hayo leo Agosti 01, 2026, alipotembelea banda la TAFICO katika Maonesho ya Nanenane 2026 yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samuel Malecela, Nzuguni jijini Dodoma, ambapo alipokea maelezo kuhusu shughuli na uwekezaji unaotekelezwa na Shirika kutoka kwa Afisa Mtendaji Mkuu wa TAFICO, CPA Shaibu Matessa.

Akizungumza mara baada ya kupokea maelezo hayo, Mhe. Dkt. Mwigulu alisema Serikali imeonesha kwa vitendo dhamira ya kuibadili sekta ya uvuvi kupitia uwekezaji wa kimkakati katika miundombinu na vitendea kazi.

"Kupitia uwekezaji huu wa vitendea kazi na miundombinu tunaiona dhamira ya Serikali kwa vitendo katika kuibadilisha sekta hii ya uvuvi iwe ya kibiashara basi niseme tuu Songeni mbele," alisema Waziri Mkuu.

Awali, CPA Matessa alimweleza Waziri Mkuu kuwa Serikali imeendelea kuandika historia katika sekta ya uvuvi kupitia uwekezaji mkubwa utakaoiwezesha TAFICO kupata meli za kisasa za uvuvi wa bahari kuu pamoja na ujenzi wa Bandari ya Uvuvi, ambayo itakuwa kitovu cha shughuli za uvuvi wa bahari kuu nchini.

"Mhe. Waziri Mkuu mpaka sasa Shirika lina meli moja ya uvuvi wa Bahari Kuu na uwepo wa bandari ya uvuvi ambao umekamilika hivi vyote ni vitendea kazi muhimu katika kuleta mapinduzi ya Sekta ya Uvuvi na kuwa ya kibiashara".Alisema CPA.Matessa

Mabadiliko haya ya kisekta yanalenga kuongeza mchango wake katika uzalishaji wa mazao ya uvuvi, uchakataji na kuimarisha mnyororo wa thamani kwa mazao ya uvuvi na kuongeza ajira kwa wanawake na vijana.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba akizungumza na uongozi wa Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO)  alipotembelea banda la Shirika hilo katika maonesho ya Nanenane yanayofanyika katika Viwanja vya Nzuguni, jijini Dodoma
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba  akisikiliza maelezo kutoka kwa Afisa Mtendaji Mkuu wa TAFICO, CPA Shaibu Matessa alipotembelea banda la Shirika hilo katika maonesho ya Nanenane yanayofanyika katika Viwanja vya Nzuguni, jijini Dodoma

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akikata utepe pamoja na Rais wa Jamhuri ya Angola Mheshimiwa João Manuel Gonçalves Lourenço kama ishara ya uzinduzi wa Hospitali Kuu ya Rufaa ya Rais Julius Nyerere (Hospital dos Queimados Presidente Julius Nyerere) iliyopo Kilamba, jijini Luanda, Angola, tarehe 01 Agosti, 2026. Kulia ni Mama Maria Nyerere, Mjane wa Baba wa Taifa akishuhudia tukio hilo. Hospitali hiyo imepewa jina la Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, kama heshima na ishara ya kutambua mchango wake katika harakati za ukombozi wa Bara la Afrika, hususan nchi za Kusini mwa Afrika, ikiwemo Angola.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na Rais wa Jamhuri ya Angola, Mheshimiwa João Manuel Gonçalves Lourenço, Mjane wa Baba wa Taifa Mama Maria Nyerere pamoja na viongozi mbalimbali wakati wakifuatilia Makala Maalum ya Hospitali Kuu ya Rufaa ya Rais Julius Nyerere (Hospital dos Queimados Presidente Julius Nyerere) pamoja na Historia ya Baba wa Taifa kabla ya uzinduzi wa Hospitali hiyo iliyopo Kilamba, jijini Luanda, Angola, tarehe 01 Agosti, 2026.

Taswira ya Hospitali Kuu ya Rufaa ya Rais Julius Nyerere (Hospital dos Queimados Presidente Julius Nyerere) iliyopo Kilamba, jijini Luanda, nchini Angola.
Taswira ya Hospitali Kuu ya Rufaa ya Rais Julius Nyerere (Hospital dos Queimados Presidente Julius Nyerere) iliyopo Kilamba, jijini Luanda, nchini Angola.

Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Ukusanyaji Mapato Tanzania (TAREWU) Wakili na CPA Dkt.Michael Marere na Mkurugenzi Mtendaji wa Global Dynamic Consulting (GDC)  Anne Massawe wakisaini hati za makubaliano katika hafla iliyofanyika Ofisi za GDC  jijini Dar es Salaam.
Mkuugenzi wa  Mtendaji wa Global Dynamic Consulting Anne Massawe akizungumza namna watavyoshirikiana na  TAREWU katika makubaliano ya usimamizi wa miradi ya maendeleo ya uongozi.
Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Ukusanyaji Mapato Tanzania (TAREWU) Dkt.Michael Marere akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana TAREWU kuingia makubaliano na Global Dynamic  Consulting  (GDC)  kwa ajili ya usimamizi wa miradi ya maendeleo na uongozi.

Baadhi ya matukio katika picha mara baada ya kusaini makubaliano
Na Mwandishi Wetu
CHAMA cha Wafanyakazi Wakusanya Mapato Tanzania (TAREWU) kimesaini Hati ya Makubaliano (MoU) na Global Dynamics Consulting (GDC), kwa lengo la kuimarisha uwezo wa wanachama wake katika usimamizi wa miradi na maendeleo ya uongozi.

Ushirikiano huo unalenga kuwawezesha wafanyakazi na viongozi kupata ujuzi, maarifa na uwezo wa kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya taasisi zao na taifa kwa ujumla.

Akizungumza mara baada ya kusaini hati hiyo, Katibu Mkuu wa TAREWU, Wakili na CPA Dkt. Michael Marere, amesema ushirikiano huo ni sehemu ya mkakati mpana wa chama wa kuwajengea wanachama uwezo na kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya kitaaluma na kiuchumi.

Amesema TAREWU itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha wanachama wanapata fursa za kuongeza ujuzi, kubadilishana uzoefu na kunufaika na programu zinazolenga kuimarisha uwezo wao.

Dkt. Marere amesema makubaliano hayo yatawezesha taasisi hizo mbili kuandaa na kutekeleza programu mbalimbali za mafunzo, semina na shughuli nyingine zinazolenga kuongeza uwezo wa wafanyakazi na viongozi katika maeneo mbalimbali.

Amesema ushirikiano na GDC pia utalenga kuandaa programu za kukuza uongozi wenye ufanisi, kuimarisha uwezo wa viongozi katika taasisi mbalimbali na kuwajengea uwezo wa kukabiliana na changamoto zinazojitokeza katika utekelezaji wa majukumu yao.

Kwa mujibu wa TAREWU, upatikanaji wa viongozi wenye uwezo ni muhimu katika kuhakikisha taasisi zinafanya kazi kwa ufanisi na kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi.

Chama hicho kimesema mazingira ya sasa yanahitaji viongozi wenye uwezo wa kufanya maamuzi sahihi, kusimamia rasilimali kwa ufanisi na kuongoza mabadiliko yanayolenga kuboresha utendaji wa taasisi.

Aidha, TAREWU imesisitiza umuhimu wa kuendelea kuwekeza katika mafunzo na maendeleo ya viongozi ili kuwawezesha kukabiliana na changamoto zinazotokana na mabadiliko ya kijamii, kiuchumi na kiteknolojia.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Global Dynamics Consulting (GDC), Anne Massawe, amesema kampuni hiyo ina dhamira ya kuendelea kusaidia taasisi mbalimbali kuimarisha mifumo bora ya uongozi na kuongeza uwezo wa utekelezaji wa miradi.

Massawe amesema kusainiwa kwa hati hiyo ni hatua muhimu katika kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi hizo, huku akisisitiza umuhimu wa kuwekeza katika maendeleo ya rasilimali watu kwa manufaa ya wanachama na jamii kwa ujumla.

Chini ya makubaliano hayo, TAREWU na GDC zinatarajia kutekeleza programu za kujenga uwezo katika usimamizi wa miradi na uongozi, warsha na semina za mafunzo, programu za uelekezi na ushauri elekezi kwa wanachama, pamoja na mijadala ya kubadilishana maarifa.

Shughuli nyingine zitakazotekelezwa ni pamoja na kutoa fursa za kujenga mitandao ya kitaalamu, tafiti na ubunifu unaolenga kuongeza uelewa na kuboresha utendaji wa taasisi.

Taasisi hizo zimesema juhudi hizo zinalenga kuhakikisha viongozi wanakuwa na maarifa, ujuzi na mtazamo unaowawezesha kuleta matokeo chanya katika taasisi wanazoziongoza.

Na Mwandishi Wetu
CHUO cha Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi na Huduma VETA Chang’ombe, Dar es Salaam, kimesema mafunzo ya ubunifu wa mavazi na mitindo yanaendelea kuwa chachu ya kuwawezesha vijana kujiajiri, kuajiri wengine na kuchangia katika kupunguza tatizo la ukosefu wa ajira nchini.

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Chuo cha VETA Chang’ombe, Abraham Richard Mbughuni, wakati wa onyesho la kazi za wanafunzi wa mwaka wa tatu wa kozi ya Diploma ya Ubunifu wa Mavazi na Mitindo, ambapo wanafunzi waliwasilisha kazi zao ikiwa ni sehemu ya mtihani wa mwisho.

Mbughuni alisema ubunifu ulioonyeshwa na wanafunzi hao ni kielelezo cha maarifa na ujuzi walioupata chuoni, huku akieleza kuwa unathibitisha jitihada za VETA katika kuzalisha wahitimu wenye uwezo wa kushindana katika soko la ajira ndani na nje ya nchi.

Alisema Serikali imeendelea kuwekeza katika elimu ya ufundi na stadi kupitia VETA, hatua inayowawezesha vijana kupata ujuzi wa kujitegemea badala ya kutegemea ajira rasmi ambazo mahitaji yake ni makubwa kuliko nafasi zilizopo.

“Kila ubunifu na muundo wa vazi unaoonyeshwa ni msingi wa ajira za baadaye na unaweza kuwa nembo ya Tanzania katika sekta ya ubunifu. Wanafunzi hawa si wahitimu pekee, bali ni wajasiriamali na waajiri wa kesho,” alisema.

Mbughuni aliwataka wadau mbalimbali kuendelea kuunga mkono sekta ya ubunifu wa mavazi kwa kuweka mazingira bora yatakayowezesha sekta hiyo kukua.

Alisema iwapo vyuo vya VETA vitaendelea kuzalisha wabunifu wengi kila mwaka, Tanzania itaongeza uwezo wa kuzalisha mavazi yake yenyewe na kupunguza utegemezi wa bidhaa kutoka nje.

Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Textile and Fashion Design katika VETA Dar es Salaam, Josephat Maghina, alisema onyesho hilo lilikuwa sehemu ya mtihani wa mwisho wa wanafunzi, ambapo kila mwanafunzi alitakiwa kuandaa mkusanyiko wa mavazi matano yaliyobuniwa kutokana na wazo au msukumo aliouchagua.

Maghina alisema mafunzo ya sasa yanazingatia ubunifu wa kisasa unaoanzia katika utafiti, uchoraji wa michoro, maandalizi ya kazi hadi utengenezaji wa mavazi, tofauti na mtazamo wa zamani wa kushona bila kufuata mchakato wa kitaalamu.

Alisema kozi hiyo inawawezesha wahitimu kujiajiri, kuajiriwa katika taasisi mbalimbali na kuanzisha biashara zao, huku akiwahimiza vijana wenye sifa kujiunga na VETA ili kunufaika na fursa zinazopatikana katika sekta ya mitindo na mavazi.

“Mahitaji ya wabunifu wa mavazi yanaendelea kuongezeka kutokana na ukuaji wa tasnia hii. Wahitimu wetu wana uwezo wa kushiriki katika matukio makubwa ya kitaifa na kimataifa, ikiwemo kubuni mavazi kwa viongozi na mashindano mbalimbali,” alisema Maghina.

Mhitimu wa kozi hiyo, Andrea Johannes, alisema mafunzo aliyoyapata yamemjengea uwezo wa kuingia kwa kujiamini katika soko la ajira, akieleza kuwa lengo lake ni kujiajiri na baadaye kuajiri vijana wengine baada ya kuanzisha karakana yake ya ushonaji.

Naye mhitimu, Beatrice Richard Mahimbo, alisema ujuzi walioupata kutoka kwa wakufunzi wa VETA umewapa msingi wa kujitegemea kiuchumi, huku akiahidi kuwahamasisha vijana wengine kujiunga na kozi hiyo ili kuongeza idadi ya wabunifu wenye uwezo nchini.

Jumla ya wanafunzi 27 wamehitimu mafunzo ya Diploma ya Ubunifu wa Mavazi na Mitindo, huku uongozi wa chuo ukieleza kuwa una imani wahitimu hao watakuwa sehemu ya nguvu kazi itakayochochea maendeleo ya sekta ya mitindo, kuongeza ajira na kuunga mkono juhudi za Tanzania za kujenga tasnia imara ya mavazi







Top News