Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA) itashiriki katika Maonesho ya Kilimo ya Nanenane Kitaifa 2026 yatakayofanyika kuanzia tarehe 1 Agosti 2026 kwenye viwanja vya Dkt. John Malecela, Dodoma, ikiwa na mpango maalumu wa kuwaunganisha wadau wa sekta ya nafaka na mazao mchanganyiko na fursa za masoko, biashara, teknolojia na uongezaji thamani.
Ushiriki wa COPRA unaendana na kaulimbiu ya Nanenane 2026, “Tambua Soko; Ongeza Tija Kutekeleza Dira 2050,” kwa kuweka msisitizo katika uzalishaji unaozingatia mahitaji ya soko, ubora wa mazao, biashara rasmi, uongezaji thamani na matumizi ya teknolojia ili kuongeza tija na ushindani wa mazao ya Tanzania.
Banda la COPRA litakuwa kitovu cha maarifa, huduma, biashara na ubunifu, ambapo wakulima, wafanyabiashara, wasindikaji, wawekezaji, vijana na wananchi kwa ujumla watapata elimu na ushauri wa kitaalamu kuhusu masoko ya ndani na kimataifa, viwango vya ubora, mifumo rasmi ya biashara, uongezaji thamani, teknolojia na huduma za kidijitali kupitia mfumo wa COPRAMIS.
Kipekee katika Nanenane 2026, COPRA itaandaa Warsha Maalumu ya Zao la Mahindi itakayofanyika tarehe 5 Agosti 2026. Warsha itakutanisha wadau kujadili uwekezaji kwenye uzalishaji, masoko, biashara, fedha na mitaji, uongezaji thamani na ushindani wa zao hilo.
Aidha, tarehe 7 Agosti 2026, kutakuwa na siku ya watengeneza maudhui ya biashara ya mazao mtandaoni ‘Digital Agribusiness Influencers Day’, na kuwakutanisha na Mamlaka na kutoa fursa ya kupata ufahamu wa masoko na biashara rasmi ya nafaka na mazao mchanganyiko ili kuunganisha na kutumia nguvu ya mawasiliano katika kukuza taarifa za masoko, fursa za biashara, teknolojia na ubunifu.
Mkurugenzi Mkuu wa COPRA, Bi. Irene Madeje Mlola, amesema ushiriki wa Mamlaka mwaka huu umejikita katika kuhakikisha wadau wanapata maarifa, taarifa sahihi, uelewa huduma na fursa zinazowawezesha kufanya maamuzi bora katika uzalishaji na biashara ya nafaka na mazao mchanganyiko.
“Tunataka kila mdau anayefika Banda la COPRA aondoke akiwa na uelewa wa uzalishaji wenye tija, viwango, ubora, soko na fursa zinazoweza kumsaidia kuongeza tija na thamani ya mazao yake.
Sambamba na kutafuta masoko ya nje, tunataka pia kuhamasisha matumizi na uongezaji thamani wa mazao yetu hapa nchini ili kujenga soko imara la ndani na kuongeza fursa kwa wakulima na wafanyabiashara,” amesema Bi. Mlola.
COPRA inawakaribisha wakulima, wafanyabiashara, wasindikaji, wawekezaji, vijana na wananchi kwa ujumla kutembelea Banda la COPRA kuanzia tarehe 1 Agosti 2026, kupata huduma na ushauri wa kitaalamu, kutambua fursa za masoko na biashara, kujifunza kuhusu matumizi na uongezaji thamani wa mazao, pamoja na kujenga mitandao ya biashara.
Pia, COPRA itakuwa na eneo maalumu la vyakula vya lishe vinavyotokana na mazao yanayosimamiwa na Mamlaka, likiwa na lengo la kuhamasisha matumizi ya mazao yanayozalishwa nchini, hususan mikunde kama choroko, dengu na mbaazi.
Kupitia maonesho ya mapishi na vyakula mbalimbali, wageni watajifunza namna mazao hayo yanavyoweza kutumika katika mlo wa kila siku, huku yakifungua fursa za uongezaji thamani, biashara na kupanua soko la ndani kwa mazao ya wakulima.
Nanenane 2026: Tambua Soko; Ongeza Tija Kutekeleza Dira 2050.
Mkurugenzi Mkuu wa Copra, Bi Irene Madeje Mlola.


.jpeg)


.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)



.jpeg)










.jpeg)
.jpeg)



















