Fikiria unatua katika nchi mpya na intaneti yako tayari inafanya kazi kabla hata hujatoka uwanja wa ndege. Hakuna haja ya kutafuta Wi-Fi. Hakuna kununua SIM card ya ndani. Wala kulipa gharama kubwa za kutumia huduma ya intaneti ukiwa nje ya nchi (roaming).

Programu mpya ya Kwetu eSIM inamwezesha mtu yeyote kununua kifurushi cha intaneti kwa ajili ya safari kabla ya kusafiri na kukiwasha ndani ya chini ya dakika moja. Hakuna SIM card ya kawaida ya kubadilisha, hakuna kifaa kidogo cha kufungulia sehemu ya SIM card cha kubeba, wala foleni katika maduka ya huduma za simu uwanja wa ndege. Unachotakiwa kufanya ni kuchagua unakokwenda, kufanya malipo, kuskani QR code au kuingiza msimbo wa usajili, na kuanza kutumia intaneti katika nchi zaidi ya 190. Kwetu eSIM inakubali malipo kwa kadi pamoja na huduma za fedha kwa njia ya simu, ikiwemo Airtel Money na Mix, kupitia DPO na pochi ya fedha ndani ya programu. Kwetu eSIM inafanya kazi kwenye simu za iPhone na Android na inatumia lugha mbalimbali, hivyo kurahisisha huduma kwa wasafiri kutoka maeneo mbalimbali duniani. Hakuna SIM card. Hakuna usumbufu wa roaming. Unatua tu na kuunganishwa. Programu ya Kwetu eSIM sasa inapatikana kwenye Apple App Store na Google Play, huku vifurushi vya intaneti kwa ajili ya safari vikiweza pia kununuliwa kupitia kwetuesim.com. Kwa maelezo zaidi, tembelea kwetuesim.com au https://kwetuesim.com/sw/

KUTAZAMA VIDEO BONYEZA HAPA

Dar es Salaam, Agosti 31, 2026 Serikali ya Somalia imeendelea kuchukua hatua za kuimarisha mageuzi ya utumishi wa umma kwa kujipanga kuanzisha Chuo cha Taifa cha Utumishi wa Umma huku ikilenga kutumia uzoefu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) katika uendeshaji wa taasisi ya mafunzo ya watumishi wa umma.Hayo yameelezwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Shirikizo ya Somalia, Mhe. Hirsi Jama Ganni ulipotembelea Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) akiongoza ujumbe wa serikali hiyo ikiwa ni sehemu ya ziara rasmi ya siku nne nchini Tanzania iliyolenga kujifunza uzoefu wa Tanzania katika mageuzi ya sekta ya umma, mabadiliko ya kidijitali na maboresho ya mifumo ya Serikali.


Mhe. Ganni amesema Somalia imeweka mageuzi ya utawala wa umma kuwa moja ya vipaumbele vya kitaifa na kwamba mafanikio ya Serikali yanategemea kuwa na watumishi wenye ujuzi na uwezo wa kubadilisha sera na mipango kuwa matokeo halisi kwa wananchi.

“Somalia inapanga kuanzisha Chuo cha Taifa cha Utumishi wa Umma kitakachokuwa na jukumu la kutoa mafunzo kwa watumishi wa Serikali, kuanzia mafunzo ya awali kwa watumishi wapya hadi mafunzo kwa viongozi waandamizi. amesema Mhe. Ganni”

Mhe. Ganni ameongeza kuwa Tanzania imejenga mfumo ambao Somalia kwa sasa inalenga kuuanzisha, hivyo ziara hiyo imekuwa muhimu kwao katika kujifunza namna TPSC inavyoandaliwa, jinsi mitaala inavyotengenezwa na kusasishwa, pamoja na namna taasisi inavyoweza kuendelea kuwa na umuhimu katika kukabiliana na mabadiliko ya vipaumbele vya Serikali.

“Tuna matumaini ziara hii itakuwa mwanzo wa ushirikiano wa muda mrefu katika maeneo ya uandaaji wa mitaala, kubadilishana wakufunzi na uzoefu, ujenzi wa taasisi pamoja na matumizi ya majukwaa ya kidijitali katika mafunzo,” amesema Mhe. Ganni
Akizungumzia ziara hiyo, Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu wa TPSC, Dkt. Ernest Mabonesho, amesema ujumbe huo umetembelea Tanzania kwa lengo la kujifunza namna utumishi wa umma unavyoendeshwa nchini, huku ziara ya TPSC ikiwa na msisitizo wa kujifunza kuhusu uanzishwaji na uendeshaji wa chuo cha utumishi wa umma.

Dkt. Mabonesho amesema Somalia ilikuwa na chuo cha utumishi wa umma hapo awali, lakini taasisi hiyo ilishindwa kuendelea kufanya kazi kutokana na changamoto zilizotokana na vita, hivyo sasa nchi hiyo inapanga kuanzisha upya taasisi hiyo kwa kujifunza kutoka nchi mbalimbali ikiwemo Tanzania.

Ameeleza kuwa mafunzo ya utumishi wa umma ni muhimu kwa kuwaunganisha wataalamu kutoka kada mbalimbali wanaohudumu katika Serikali, wakiwemo madaktari, wahandisi na wahasibu, ili wote wawe na uelewa wa maadili, wajibu na namna bora ya kuwahudumia wananchi kwa heshima na staha.

Katika hatua nyingine, Dkt. Mabonesho amesema ziara hiyo imekuwa na manufaa pia kwa TPSC kutokana na uzoefu na maswali yanayotolewa na wageni hao, ambayo yanaweza kusaidia Chuo kutafakari na kuboresha baadhi ya maeneo ya utendaji.

Amesema miongoni mwa maeneo yaliyovutia mjadala ni utaratibu wa baadhi ya nchi kuwapatia watumishi wa umma mafunzo na mitihani kabla ya kuingia rasmi katika utumishi wa umma, akieleza kuwa suala hilo linaweza kusaidia kuwaandaa watumishi kabla ya kuanza kutekeleza majukumu yao.








 


SHIRIKA la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) limetoa wito kwa sekta binafsi kuongeza uwekezaji katika bandari kavu, maeneo ya kuhifadhi makontena na miundombinu ya maegesho ya malori ili kukabiliana na ongezeko la mizigo inayopita katika Bandari ya Dar es Salaam.

TASAC imesema ongezeko la idadi ya makontena yanayohudumiwa katika Bandari ya Dar es Salaam linatokana na kuimarika kwa mazingira ya uwekezaji pamoja na maboresho yaliyofanyika katika huduma za bandari.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa TASAC, Mohamed Salum, amesema kuongezeka kwa shughuli za bandari kumeongeza mahitaji ya malori na maeneo ya kuhifadhi makontena.

Amesema maboresho hayo yameongeza ufanisi wa huduma za bandari, ikiwemo kupunguza muda wa 
kuhudumia meli na upakuaji wa makontena.

Kwa mujibu wa TASAC, mwezi Julai pekee Bandari ya Dar es Salaam ilihudumia takribani makontena 137,000, hali inayoonyesha kuongezeka kwa shughuli za biashara kupitia bandari hiyo.

TASAC imeeleza kuwa ongezeko hilo linahitaji maandalizi zaidi katika miundombinu ya usafirishaji na uhifadhi wa makontena, hususan kuongeza idadi ya malori na maeneo ya bandari kavu.

“Wenye bandari kavu wanapaswa kuongeza maeneo kwa ajili ya malori. Hii ni fursa na siyo laana,” imeelezwa.

Shirika hilo pia limewataka wamiliki wa bandari kavu kupanua maeneo ya maegesho ya malori na kuongeza uwezo wa kuhifadhi makontena ili kusaidia kupunguza msongamano katika maeneo ya bandari.

TASAC imesisitiza kuwa ongezeko la makontena ni fursa ya kiuchumi inayopaswa kuungwa mkono na sekta binafsi kupitia uwekezaji katika bandari kavu, malori na maeneo ya kuhifadhi makasha.

Aidha, TASAC imeonya dhidi ya taarifa na kauli zinazoweza kutoa taswira hasi kuhusu shughuli za Bandari ya Dar es Salaam, ikisema baadhi ya kauli zinaweza kupotosha mafanikio yaliyopatikana katika kuboresha huduma za bandari.

Kwa upande mwingine, TASAC imeeleza kuwa kwa kushirikiana na waendeshaji wa bandari, ikiwemo DP World, uwezo wa kuhudumia meli umeongezeka, huku baadhi ya meli kubwa zikihudumiwa ndani ya muda mfupi.

Meneja wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), Abed Gallus, amesema mamlaka hiyo inaendelea kujiandaa kukabiliana na ongezeko la mizigo kwa kuboresha uwezo wa kuhifadhi na kuhamisha makontena kutoka eneo moja kwenda jingine ndani ya bandari.

TASAC imeeleza kuwa meli yenye takribani makontena 3,000 inaweza kuhudumiwa ndani ya siku moja, hatua inayosaidia kupunguza muda wa meli kukaa bandarini na kuongeza ufanisi wa usafirishaji wa mizigo.

Katika kipindi cha miaka miwili iliyopita, shughuli za Bandari ya Dar es Salaam zimeendelea kukua, huku ongezeko la mizigo likiongeza mahitaji ya miundombinu ya usafirishaji na uhifadhi.

Katika upande wa bandari kavu, Bandari Kavu ya Kwala ina uwezo wa kuhudumia takribani makontena 300,000 kwa mwaka, huku taarifa zikitaja kuwa uwezo wake wa kuhifadhi na kuhudumia makontena unahitaji kuendana na ongezeko la mizigo inayopita katika Bandari ya Dar es Salaam.

Aidha, takribani makontena 1,350 yaliyopo Bandari Kavu ya Kwala yanahitaji kuondolewa ili kuongeza nafasi ya kuhifadhi na kuwezesha bandari hiyo kuendelea kuhudumia mizigo inayoongezek


-AWATAKA WATUMISHI KUACHA KUFANYA KAZI KWA MAZOEA

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius Ndejembi, amewataka watumishi wa Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira kuongeza bidii, uwajibikaji na kuachana na utendaji wa kazi kwa mazoea ili kuhakikisha majukumu ya Serikali yanatekelezwa kwa ufanisi na kwa wakati.

Makamu wa Rais ametoa wito huo leo, alipofanya ziara yake ya kwanza katika Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), iliyopo Mtumba, jijini Dodoma, ambako alipokelewa na wafanyakazi pamoja na Menejimenti ya Wizara hiyo.

Amesisitiza umuhimu wa watumishi kubadili mitazamo na namna ya kufanya kazi, akitaka kila mmoja kuwa mbunifu na kuweka mipango inayolenga kuleta matokeo yanayoonekana kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.

Makamu wa Rais amewasihi watumishi kutumia nafasi zao kutoa huduma yenye thamani kwa watanzania na kutambua dhamana waliyonayo katika kuwahudumia wananchi. Pia amewataka kubadili mitazamo na namna ya kufikiri, kuwa wabunifu na kuhakikisha mipango inayowekwa inaleta tija na matokeo chanya katika shughuli mbalimbali zinazotekelezwa kwa maslahi mapana ya Taifa.

Halikadhalika, amewataka kuongeza jitihada katika kudumisha Muungano kwa kuwa na mipango endelevu inayolenga kutatua changamoto mbalimbali pamoja na kutoa elimu ya fursa zilizopo katika Muungano.

Amewasihi Viongozi na Watumishi wa Wizara hiyo, kuwa na mipango endelevu katika utekelezaji wa ajenda ya ulinzi na uhifadhi wa mazingira kwa kutumia vema kampeni za upandaji miti, usafi wa majiji na miji kwa kuweka nyenzo zitakazosaidia kufanya hali hiyo kuwa endelevu. Vile vile amesisitiza umuhimu wa kuwa na Mpango maalum utakao saidia wananchi kuhama katika shughuli za kila siku zinazoharibu mazingira.

Awali, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhandisi Hamad Masauni, amempongeza Makamu wa Rais kwa kuaminiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika nafasi hiyo na kumhakikishia ushirikiano katika kutekeleza majukumu mbalimbali yanayohusu Ofisi ya Makamu wa Rais.

Akiwasilisha taarifa kuhusu shughuli zinazotekelezwa na idara mbalimbali zilizo chini ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Richard Muyungi, amesema wizara hiyo ina Idara nne, Vitengo nane na Taasisi mbili zinazotekeleza majukumu mbalimbali, ikiwemo utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 katika masuala ya Muungano na Mazingira.






Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita linamshikilia Jackline Peter, mkazi wa Mji Mdogo wa Katoro, Wilaya na Mkoa wa Geita, kwa tuhuma za kumshambulia kwa fimbo Rahel Jumanne baada ya kumtilia shaka kumwibia fedha.

Akitoa taarifa hiyo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita amesema tukio hilo la kikatili lilitokea tarehe 26 Agosti 2026, saa 5.00 asubuhi nyumbani kwa mtuhumiwa Katoro.

Inadaiwa mtuhumiwa aligundua amepoteza fedha kiasi cha Shilingi 60,000/= zilizokuwa kwenye pochi chumbani kwake. Baada ya hapo alimtilia shaka Rahel Jumanne aliyekuwa amemtembelea kwake.

Kamanda amesema baada ya fedha hizo kudaiwa kupotea, mtuhumiwa alimkamata mwathirika na kuanza kumshambulia kwa fimbo.

Katika tukio hilo, mfanyakazi wa kazi za ndani wa mtuhumiwa alielekezwa kurekodi vitendo hivyo kwa kutumia simu ya mtuhumiwa. Baadaye mtuhumiwa mwenyewe alisambaza picha mjongeo hiyo kwenye mitandao ya kijamii.

Baada ya Jeshi la Polisi kubaini tukio hilo kwenye mitandao ya kijamii, lilifanya ufuatiliaji wa haraka na kufanikiwa kubaini eneo la tukio, kumtambua mtuhumiwa na kumkamata. Kwa sasa anaendelea kuhojiwa.

Kamanda amesema uchunguzi wa tukio hilo unaendelea na mara utakapokamilika mtuhumiwa atafikishwa katika mamlaka husika za kisheria kwa hatua zaidi.

Aidha ametoa wito kwa baadhi ya wananchi kuacha tabia ya kujichukulia sheria mkononi.

"Tuhuma za uhalifu hazimruhusu mtu kutoa adhabu mwenyewe. Mtu anatakiwa kutoa taarifa kwa mamlaka za kisheria ili hatua zichukuliwe," amesisitiza.



JESHI la Polisi mkoa wa Kilimanjaro linamshikilia Mwanafunzi wa kidato cha tatu katika shule ya sekondari Kisarika wilayani Moshi, Nelson Mkenda (17), kwa tuhuma za kumjeruhi mwanafunzi mwenzake aitwaye Vicent Mmary, (17) wa shule ya Sekondari Kisarika, kidato cha tatu kwa kitu chenye ncha kali kifuani na kusababisha kifo chake.

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro, SACP Saimon Maigwa alisema kuwa, tukio hilo limetokea Agosti 28 mwaka huu majira ya saa tisa na robo alasiri huko katika shule ya Sekondari Kisarika, kitongoji cha Manushi, kijiji cha Ongomauru, Kata ya Uru Kaskazini, Wilaya ya Moshi.

Alisema kuwa, ulitokea ugonvi baina yao baada ya Marehemu kumtuhumu Mtuhumiwa kuiba vitu mbalimbali kwenye mabweni ya shule hiyo.

Mwanafunzi huyo alifariki dunia akiwa njiani kuelekea hospitali ya Rufaa ya Mkoa ya Mawenzi kwa matibabu.

Uchunguzi wa kina unaendelea ili kukamilisha taratibu za kisheria na kumfikisha mtuhumiwa Mahakamani.

Na Janeth Raphael - MichuziTv


Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimeendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuimarisha uzalishaji wa mapato ya ndani kwa kuanzisha kampuni ya uwekezaji itakayoratibu na kusimamia vitengo mbalimbali vya uzalishaji visivyo vya kitaaluma, hatua inayolenga kuongeza ufanisi, tija na uwezo wa Chuo kujiendesha kibiashara.

Akizungumza na vyombo vya habari kuhusu mafanikio ya SUA katika kipindi cha Awamu ya Sita, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu hicho, Prof. Raphael Chibunda, amesema SUA kupitia kampuni yake ya uwekezaji ya SUA Income Generation & Services Ltd, inaendelea kutekeleza mikakati madhubuti ya kutumia rasilimali zake katika shughuli zenye uwezo wa kuzalisha mapato na kuchochea maendeleo ya Chuo.

Amesema katika kutekeleza mkakati huo, ukarabati wa majengo ya Kiwanda cha Uchapishaji (Printing Unit) pamoja na Kitengo cha Maziwa (Dairy Unit) umekamilika, huku baadhi ya mitambo ya uchapishaji ikiwa tayari imefungwa na kuwekwa katika hali ya kuanza uzalishaji.

Prof. Chibunda amesema SUA pia inaendelea kutumia mitambo ya Feed Mill & Silos kwa ajili ya uzalishaji wa chakula cha mifugo, kuku na samaki, hatua ambayo pamoja na kusaidia mahitaji ya uzalishaji wa Chuo, inalenga pia kuongeza mapato kupitia shughuli za kibiashara.

Katika kuimarisha uwekezaji wa muda mrefu, amesema SUA imeanza kutumia rasilimali zake za misitu katika fursa za uchumi wa kijani, ambapo Msitu wa Ifinga wenye ukubwa wa hekta 10,000, uliopo Wilaya ya Madaba mkoani Ruvuma, unalengwa kutumika katika biashara ya kimataifa ya hewa ukaa (Carbon Trading).

Amesema tayari hekta 1,500 za msitu huo zimepandwa miti ya biashara, hatua inayoweka msingi wa Chuo kushiriki katika soko la kimataifa la hewa ukaa huku kikihakikisha matumizi endelevu ya rasilimali za misitu.

Aidha, amesema SUA imeendelea kuwekeza katika kilimo cha mazao yenye fursa za kibiashara, ambapo katika Shamba la Biashara lililopo Kampasi ya Solomon Mahlangu, jumla ya ekari 200 za mkonge zimepandwa na ekari 100 za mwanzo tayari zimefikia hatua ya kuanza kuvunwa kwa ajili ya uzalishaji wa nyuzi za katani.

Prof. Chibunda amesema katika kuimarisha usimamizi wa shughuli hizo, mwezi Mei 2026 Baraza la Chuo liliunda Bodi ya Usimamizi na kumteua Meneja wa Mpito wa SUA Income Generation & Services Ltd, kwa ajili ya kuanza utekelezaji wa shughuli za kampuni hiyo.

Amesema kampuni hiyo inatarajiwa kuchukua na kusimamia vitengo vyote vya uzalishaji ambavyo si vya kitaaluma lakini vina uwezo mkubwa wa kuzalisha mapato kwa Chuo, ikiwemo Shamba la Biashara la Kampasi ya Solomon Mahlangu pamoja na vitengo vyake vya maziwa, nguruwe, malisho, shamba na uzalishaji wa chakula cha mifugo.

Vitengo vingine vinavyolengwa kuingia katika uwekezaji huo ni pamoja na Kiwanda cha Samani cha Vuyisile (Vuyisile Mini Furniture Factory) kilichopo Kampasi ya Solomon Mahlangu na SUA Printing Press kilichopo Kampasi ya Edward Moringe.

Kwa upande mwingine, amesema maghala mawili yaliyopo Kampasi ya Solomon Mahlangu yako katika mpango wa ukarabati ili yaweze kutumika kuanzisha kiwanda kidogo cha kuchakata matunda na kuzalisha bidhaa mbalimbali zikiwemo sharubati, maji ya kunywa pamoja na tomato sauce.

Mbali na shughuli hizo, Prof. Chibunda amesema SUA imeendelea kuwekeza katika maeneo mengine ya kimkakati kwa ajili ya kuimarisha shughuli za kitaaluma na kuongeza mapato ya ndani, ikiwa ni pamoja na uzalishaji wa chakula cha samaki na mifugo pamoja na uzalishaji wa matofali kwa ajili ya mafunzo na biashara.

Amesema Chuo pia kinaendelea kupanda miti na kununua vifaa vya kisasa vya kukatia magogo katika eneo lake la Msitu wa Mafunzo wa Olmotonyi jijini Arusha, huku kikiboresha Shamba la Mafunzo la Mfano kwa ajili ya kutoa mafunzo ya vitendo kwa wanafunzi, wakulima na wadau wengine.

Kwa mujibu wa Prof. Chibunda, Shamba hilo pia linatumika kama chanzo cha mapato ya ndani kupitia uzalishaji na uuzaji wa miche, matunda, mbogamboga, maziwa, vifaranga vya samaki na bidhaa nyingine za kilimo. Shamba hilo lina mazao na mifugo inayowakilisha kanda mbalimbali za Tanzania, ikiwemo samaki, ng’ombe, mbuzi, kuku, kondoo, ngamia, farasi na sungura.

Aidha, SUA imeendelea kuboresha miundombinu yake katika maeneo mbalimbali, ikiwemo majengo ya Morning Sight kwa ajili ya shughuli za utalii, pamoja na majengo ya Chuo yaliyopo mjini ambayo yanalengwa kutumika katika shughuli mbalimbali za kuongeza mapato.

Katika sekta ya afya, Prof. Chibunda amesema Chuo kimeendelea kuboresha Hospitali ya SUA kwa kuongeza miundombinu ya kutolea huduma, ikiwemo ujenzi wa wodi za wagonjwa na ununuzi wa vifaa tiba, hatua inayolenga kuongeza uwezo wa hospitali hiyo kutoa huduma bora kwa jamii.

Amesema uwekezaji huo ni sehemu ya mkakati mpana wa SUA wa kutumia ipasavyo rasilimali ilizonazo, kuimarisha shughuli za kitaaluma na uzalishaji, kuongeza vyanzo vya mapato na kujenga uwezo wa Chuo kujiendesha kwa ufanisi zaidi kupitia shughuli za kibiashara na uzalishaji wa ndani.



NA MWANDISHI WETU, DODOMA

Makamu wa Rais, Deogratius Ndejembi, ameelezwa kuwa kiongozi mahiri, muadilifu na mzalendo, mwenye uwezo wa kumsaidia majukumu Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.

Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Taifa, Mary Chatanda, Agosti 30, 2026, ofisini kwake Dodoma, siku moja baada ya kukamilika uapisho wa kiongozi huyo, Ikulu ya Chamwino, Dodoma.

Chatanda ameeleza, Ndejembi ni kiongozi wa vitendo na katika majukumu aliyoaminiwa tangu akiwa Mkuu wa wilaya ya Kongwa, Mbunge, Naibu Waziri na Waziri kamili katika wizara mbalimbali.

"Kule Kongwa Dodoma akiwa Mkuu wa wilaya alifanya kazi nzuri na katika kilimo alisimamia kwa mafanikio makubwa kampeni yake aliyoiita ONJAKO yaani Ondoa Njaa Kongwa. Alihimiza wananchi kulima mazao yanayostahimili ukame kama mtama, mihogo, ufuta na alizeti ili kuwaepusha wananchi na kadhia ya njaa," amesema Chatanda.

Ameongeza kuwa, kampeni ya ONJAKO ilipokelewa vizuri na wakulima wa Kongwa kutokana na mwanzo kutilia mkazo zao la mahindi ambalo mara kwa mara walikuwa wakipata mazao kidogo kutokana na changamoto ya ukame wilayani humo.

Akisisitiza utendaji uliotukuka wa Ndejembi, Chatanda amesema, Wizara kadhaa alizohudumu zikiwemo Tamisemi, Vijana, Ardhi, Nishati, ameacha alama kubwa kwa kuwa mstari wa mbele kutatua changamoto za wananchi.

"Ndejembi si mtu wa kukaa ofisini kusubiri taarifa, anakwenda mwenyewe kujionea utekelezaji wa majukumu na maagizo mbalimbali. Ndiyo maana nasema, Rais Dk. Samia amepata msaidizi mchapakazi na hodari kwelikweli," ameongeza.

Katika hatua nyingine, Mwenyekiti huyo wa UWT Taifa, ametoa rai kwa wananchi kumuombea Rais Dk. Samia, Makamu wa Rais, Ndejembi na viongozi wengine ili waweze kusimamia mipango iliyopo ambayo imejikita katika kukuza ustawi na maendeleo ya wananchi.

Awali, katika uapisho huo, Rais Dk. Samia amemuasa Makamu wa Rais Mteule kuwatumikia Watanzania bila kujali tofauti zao ili kufanikisha utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2025-2030 na Dira ya Maendeleo ya miaka 25 ijayo (2050).



Na Janeth Raphael – MichuziTv, Dodoma

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Profesa Raphael Chibunda, ameeleza kwa kina historia ya mradi wa mafunzo na utafiti wa panya unaoendeshwa na chuo hicho kwa zaidi ya miaka 25, huku akifichua namna panya shujaa Magawa alivyoweka historia duniani kabla ya kufariki.

Prof. Chibunda amezungumza hayo leo jijini Dodoma katika Mkutano na wanahabari, ambapo amesema mradi huo umekuwa ukifanyika SUA kwa zaidi ya miaka 25, ukiwalenga panya wanaofundishwa kufanya kazi mbalimbali za utafiti na huduma za kijamii, huku akibainisha kuwa panya hao wanaotumika katika mradi huo ni wa asili ya Tanzania.

Kwa mujibu wa Prof. Chibunda, panya hao walitokana na eneo la Milima ya Uluguru mkoani Morogoro, lakini kutokana na kukua kwa mradi huo, SUA kwa sasa ina kituo maalum kinachoshughulikia uzalishaji, malezi na mafunzo ya panya hao.

Amesema mfumo wa malezi na mafunzo ya panya hao umeandaliwa kwa namna ya kipekee chuoni hapo, ambapo kuna maeneo maalum kwa ajili ya panya wanaozalishwa, wanaoanza mafunzo, wanaomaliza mafunzo pamoja na wale wanaostaafu.

“Ukimfika kwetu utakuta tuna wodi ya wazazi, tuna wanaoanza mafunzo, waliohitimu, lakini pia tuna banda la panya wastaafu. Wako pale wanapata pensheni,” amesema Prof. Chibunda.


MAGAWA ALIWEKA HISTORIA CAMBODIA

Akizungumzia panya maarufu duniani Magawa, Prof. Chibunda amesema alikuwa miongoni mwa panya waliopewa mafunzo nchini Tanzania na baadaye kupelekwa Cambodia kwa ajili ya kusaidia kutambua mabomu ya ardhini.

Amesema uamuzi wa kumpeleka Magawa nchini Cambodia ulitokana na ukweli kwamba Tanzania haikuwa na changamoto kubwa ya mabomu ya ardhini kama ilivyokuwa katika baadhi ya maeneo ya nchi hiyo ya Kusini-Mashariki mwa Asia.

Magawa alifanya kazi hiyo kwa mafanikio makubwa na hatimaye kuingia katika historia ya dunia baada ya kugundua idadi kubwa ya mabomu ya ardhini, akivunja rekodi na kuwa miongoni mwa wanyama mashuhuri zaidi waliowahi kutumika katika kazi hiyo.

Uwezo wake wa kugundua mabomu ulimfanya kupata umaarufu mkubwa kimataifa, huku akitunukiwa pia nishani ya heshima kutokana na mchango wake katika kuokoa maisha ya watu na kusaidia kuondoa mabomu hatari yaliyokuwa yamesalia ardhini.


UMRI WA PANYA NA KIFO CHA MAGAWA


Prof. Chibunda amesema panya wanaofundishwa katika mradi huo wana wastani wa maisha wa takribani miaka minane, huku miaka tisa ikiwa ni hatua ya uzee mkubwa kwa panya hao.

Ameeleza kuwa wanapofikia umri huo, huanza kudhoofika kimwili na wanaweza hata kupoteza meno, hali inayowafanya kushindwa kuendelea na shughuli zinazohitaji uwezo mkubwa wa kimwili.

Magawa naye alifikia hatua hiyo ya uzee na hatimaye kufariki dunia akiwa nchini Cambodia, baada ya kutumikia kwa mafanikio katika kazi ya kutambua mabomu ya ardhini.


SUA ILITAKA MAGAWA AREJESHWE TANZANIA

Akijibu swali kuhusu iwapo kulikuwa na mpango wa kumrejesha Magawa nchini Tanzania baada ya kufariki, Prof. Chibunda amesema mpango huo uliwahi kufikiriwa, lakini changamoto za taratibu na vibali vya usafirishaji zilisababisha kutotekelezwa kwa wakati.

“Tunasema ingewezekana, lakini kwa wakati ule taratibu na vibali vya kilojistiki viligoma. Wenzetu kule Cambodia walikosa uvumilivu wa kusubiri, wakamjengea mnara mkubwa kule,” amesema Prof. Chibunda.

Kwa hatua hiyo, Magawa aliendelea kubaki nchini Cambodia ambako alifanya kazi kubwa ya kusaidia kutambua mabomu ya ardhini na kuokoa maisha ya watu.

Historia ya Magawa inaendelea kuwa sehemu muhimu ya mafanikio ya mradi wa SUA wa kufundisha panya kwa matumizi mbalimbali, ikionyesha namna utafiti unaofanywa Tanzania unavyoweza kuzalisha matokeo yenye kutambulika kimataifa.

Mradi huo pia unaendelea kuifanya SUA kuwa miongoni mwa taasisi zinazotumia utafiti na ubunifu katika kutumia uwezo wa wanyama katika kutatua changamoto za kijamii, kiafya na kiusalama.


Na Janeth Raphael - MichuziTv - Bungeni Dodoma.


Serikali imesema imeweka mikakati mbalimbali ya kukuza vipaji na ujuzi kwa vijana wenye ulemavu, kuwawezesha kupata ajira zenye staha na kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Dkt. Jafar Seif, wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Yumna Mmanga Omar, lililohusu mkakati mahsusi wa Serikali wa kukuza vipaji na ujuzi kwa vijana wenye ulemavu ili kuongeza ajira na ushiriki wao katika uchumi.

Akijibu swali hilo, Dkt. Seif amesema Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2025–2030, hususan Kifungu cha 95, imeweka msisitizo wa kuwashirikisha na kuwawezesha watu wenye ulemavu kupata ajira zenye staha pamoja na kujenga uwezo wao ili washiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi.

Amesema Serikali pia inatekeleza Mkakati wa Kitaifa wa Kukuza na Kuendeleza Vipaji na Ujuzi kwa Vijana unaoongozwa na Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Vijana ya mwaka 2007, Toleo la mwaka 2024.

Kwa mujibu wa Dkt. Seif, Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 nayo imeweka mkazo katika kukuza elimu jumuishi na kuhakikisha vijana wenye ulemavu wanapata fursa sawa katika elimu, mafunzo ya ufundi, ajira na shughuli mbalimbali za kiuchumi.

Amesema mikakati hiyo inalenga kuhakikisha ulemavu hauwi kikwazo kwa mtu kutumia kipaji, uwezo na ujuzi wake katika kujenga maisha yake na kuchangia maendeleo ya Taifa.

Katika utekelezaji wa mikakati hiyo, Serikali imewezesha vijana wenye ulemavu kupata mafunzo ya ufundi stadi katika maeneo mbalimbali nchini.

Dkt. Seif amesema jumla ya vijana 643 wenye ulemavu walijiunga na kuhitimu mafunzo ya ufundi stadi katika vyuo vitano, vikiwemo vya VETA, katika kipindi cha mwaka 2023 hadi 2025.

Amesema vijana hao walipata ujuzi katika fani mbalimbali zikiwemo umeme wa majumbani, useremala, uungaji vyuma, ushonaji wa nguo na viatu, kilimo na ufugaji, pamoja na ujenzi na uashi.

Mbali na mafunzo, Serikali imeendelea kuweka mazingira ya kuwawezesha vijana wenye ulemavu kutumia ujuzi walioupata katika kujiajiri na kushiriki katika uchumi.

Dkt. Seif amesema Serikali imetenga asilimia 30 ya zabuni za umma kwa ajili ya kuwawezesha makundi yanayolengwa, ambapo hadi mwaka 2024/25 jumla ya vikundi 703 vya watu wenye ulemavu vilikuwa vimesajiliwa katika mfumo wa NeST.

Hatua hiyo inalenga kuhakikisha kuwa ujuzi na vipaji vinavyopatikana kupitia mafunzo vinaweza kugeuzwa kuwa fursa za ajira, ujasiriamali na kujikwamua kiuchumi.

Aidha, Serikali imeendelea kutenga asilimia 10 ya mapato ya Halmashauri kwa ajili ya mikopo kwa makundi maalum, ambapo asilimia mbili hutengwa kwa ajili ya watu wenye ulemavu.

Katika kipindi cha mwaka 2021 hadi 2026, Serikali imesema jumla ya Shilingi bilioni 26.87 zimetolewa kwa ajili ya kuwawezesha watu wenye ulemavu kupitia mikopo hiyo.

Serikali imesisitiza kuwa hatua hizo ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha vijana wenye ulemavu wanapata fursa sawa za kujenga vipaji, kupata ujuzi, kuajiriwa au kujiajiri na hatimaye kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii ya Taifa.





Baraza la Masoko ya Mitaji linatarajia kuimarisha ushirikiano kwa kubadilishana uzoefu katika usimamizi wa kesi, utatuzi wa migogoro na matumizi ya teknolojia, huku shughuli za biashara na uwekezaji nchini zikiendelea kukua.

Ushirikiano huo utaliwezesha baraza la masoko ya mitaji ambalo ni baraza jipya, kujifunza kutokana na uzoefu wa baraza la ushindani  ambalo tangu lilipoanza kusikiliza migogoro mwaka 2007, limewahi kushughulikia zaidi ya kesi 525.

Maofisa wa taasisi hizo walijadili ushirikiano huo wakati ujumbe wa baraza la masoko ya mitaji ulipotembelea baraza la ushindani.

Akizungumza kuhusu ushirikiano huo Msajili wa baraza la ushindani Mbegu Kaskasi, alisema pia kubadilishana uzoefu kutasaidia taasisi hizo kuboresha huduma na kuhakikisha migogoro inayohusu wafanyabiashara na wawekezaji inatatuliwa ndani ya muda unaofaa.

“Tumekuwa hapa kwa karibu miaka 20. Wao wamekuja kujifunza kutokana na uzoefu wetu, lakini sisi pia tumejifunza mengi kutoka kwao licha ya kuwa wameanzishwa miaka mitatu iliyopita,” alisema.

Kaskasi alisema baraza hilo hushughulikia wastani wa kesi 45 hadi 50 kwa mwaka, zikiwamo zinazohusu bidhaa bandia na migogoro inayotokana na maamuzi ya mamlaka za udhibiti.

Alisema uzoefu huo unaweza kusaidia baraza la masoko ya mitaji kujenga mifumo bora ya usimamizi wa kesi kadri idadi ya wawekezaji na wafanyabiashara inavyoongezeka.

Kaskasi alisema utatuzi wa migogoro kwa haraka ni muhimu kwa sababu kesi zinazochukua muda mrefu zinaweza kuathiri thamani ya bidhaa na mali za kifedha.

“Ikiwa bidhaa zinashikiliwa kwa miaka miwili, zinaweza kuharibika. Kwa upande wa fedha, kama fedha zimefungwa na haziwezi kutumika kwa miaka miwili, thamani yake hupungua. Katika sekta ya fedha, muda ni kila kitu,” alisema.

Alisema lengo kuu la mabaraza hayo ni kuwezesha shughuli za biashara na kujenga mazingira bora zaidi kwa wawekezaji.

“Lengo la mabaraza haya ni kuchochea maendeleo ya nchi, kurahisisha biashara na kuvutia wawekezaji,” alisema.

Kwa upande wake, Msajili wa baraza la masoko ya mitaji Dk Martin Kolikoli, alisema taasisi hiyo ina nia ya kujifunza zaidi namna baraza la ushindani inavyopanga na kuratibu kesi ili kuhakikisha maamuzi yanatolewa kwa wakati.

baraza la masoko ya mitaji limekuwa likifanya kazi kwa takribani miaka mitatu na hadi sasa limesajili migogoro sita. Kesi mbili zilirudishwa kutokana na changamoto za kiutaratibu, tatu zimeamuliwa na moja bado inaendelea.

Dk Kolikoli alisema migogoro iliyowasilishwa hadi sasa imehusisha zaidi wawekezaji na wasuluhishi wa masoko ya mitaji, hususan madalali.

Alisema baadhi ya wawekezaji wamekuwa na malalamiko kuhusu maamuzi yaliyofanywa na madalali bila kuwashirikisha, huku wengine wakiwa na migogoro kuhusu fedha baada ya mauzo ya uwekezaji.

Alisema kujifunza kutoka kwa baraza lenye uzoefu zaidi kutaiwezesha baraza la masoko ya mitaji kujiandaa kwa ongezeko la kesi kadri ushiriki katika masoko ya mitaji unavyoendelea kukua.

Dk Kolikoli alisema baraza pia inaandaa mfumo wa usimamizi wa kesi utakaowawezesha wahusika kushiriki katika vikao kwa njia ya mtandao na kupata nakala za maamuzi bila kulazimika kufika katika baraza hilo.








MERIDIANBET imeendelea kuonyesha kwa vitendo dhamira yake ya kuunga mkono maendeleo ya michezo nchini baada ya kufanya zoezi jingine la uwajibikaji kwa jamii (CSR), safari hii likiwalenga vijana wa manispaa ya Tanganyika, mkoani Katavi. Kampuni hiyo imekabidhi vifaa maalum vya michezo kwa timu za Majalila FC na Kilimanjaro FC, ikiwa ni pamoja na jezi za michezo na mipira, hatua inayolenga kutoa mazingira bora zaidi ya kuendeleza vipaji vyao.

Kwa mashabiki wa soka, vifaa vya michezo si jambo dogo, kwani jezi na mpira ni sehemu muhimu ya safari ya kila mchezaji anayetaka kufika mbali. Kupitia msaada huo, Majalila FC na Kilimanjaro FC sasa wameongezewa nguvu ya kuendelea na shughuli zao za michezo huku vijana wakipata nafasi nzuri zaidi ya kujenga vipaji, nidhamu na ushindani.

Vilevile, meridianbet wana michezo mingi ya kasino mtandaoni na mechi za kimataifa za kubashiri zenye ushindani mkubwa wa odds. Jiunge leo kwa kutembelea tovuti ya meridianbet au piga *149*10# kisha uanze safari yako ya ushindi.

Akizungumza wakati wa zoezi hilo, mwakilishi wa Meridianbet, Nancy Ingram, amesema kampuni hiyo inatambua nafasi kubwa inayochezwa na michezo katika kujenga jamii yenye afya na mshikamano. “Tunatambua umuhimu wa michezo katika kuleta afya, umoja na kuimarisha mahusiano ya kijamii,” alisema Nancy Ingram, akisisitiza kuwa kampuni imeendelea kuweka nguvu katika kusaidia ukuaji wa michezo kwenye jamii mbalimbali.

Aliongeza kuwa Meridianbet inalenga kuhakikisha vijana wanapata fursa rahisi zaidi ya kushiriki michezo na kutumia vipaji vyao kwa njia chanya. Kauli hiyo inaendana na hatua mbalimbali ambazo kampuni imekuwa ikichukua katika kuunga mkono michezo na jamii, huku msaada kwa Majalila FC na Kilimanjaro FC ukiwa ujumbe mwingine kwamba maendeleo ya soka yanaanzia kwenye msingi.

Kwa ujumla, Meridianbet imefunga ukurasa mwingine wa CSR kwa alama nzuri, ikionesha kwamba mafanikio ya michezo yanahitaji ushirikiano wa wadau mbalimbali. Majalila FC na Kilimanjaro FC sasa wana vifaa vya kuongeza morali, lakini kubwa zaidi ni ujumbe kwamba vipaji vya vijana vina thamani na vinapaswa kupewa nafasi ya kukua.

WAKALI wa ubashiri Tanzania wanazidi kukukumbusha kuwa pesa hapa hazikauki, unachotakiwa kufanya wewe ni kutengeneza jamvi lako la ushindi na ubeti sasa. Arsenal, Barcelona na wengine wapo kwaajili yako.

Ligi pendwa Duniani, EPL kutakuwa na mtanange wa kukata na shoka ambapo mabingwa watetezi wa ligi hiyo Arsenal watakuwa ugenini kupepetana dhidi ya Aston Villa ambao walishangazwa kwenye mechi yao ya kwanza kwa kipigo kizito.

Vijana wa Mikel Arteta wameendelea kuuthibitishia ulimwengu kuwa mafanikio ya msi u uliyopita, hayakuja kwa bahati mbaya bali kwa kujituma na uwezo mkubwa ambao wachezaji walionesha hivyo hii mechi pia wanahitaji kwenda kufanya maajabu makubwa kabisa pale Villa Park.

Meridianbet kama kawaida wao wanampa nafasi kubwa The Gunners kuondoka na ushindi siku ya leo kutokana na kiwango ambacho anacho, lakini je vijana wa Unai watakubali kupoteza mechi ya pili mfululizo kwenye ligi?. Odds kubwa zipo hapa. Jisajili hapa.

Piga pesa kupitia michezo ya Kasino ya Mtandaoni kama vile, Keno, Aviator, Poker, Roulette, Wild Icy Fruits, Super Heli na mingine kibao. Jiunge leo kwa kutembelea tovuti ya meridianbet.co.tz au piga *149*10# kisha uanze safari yako ya ushindi.

Takwimu zinaonesha kuwa msimu uliopita kwenye mechi mbili walizokutana, kila mtu alishinda nyumbani kwake, hivyo kila timu iliondoka na pointi 3 kwenye mechi mbili walizokutana. Je safari hii itakuwaje?

Arsenal wamejiimarisha sana kwenye msimu huu kwa kuleta wachezaji wenye uwezo mkubwa akiwemo Tzolis ambaye alionesha kiwango bora kabisa kwenye mechi ya kwanza na wachezaji wengine wakifanya vyema kabisa na kuihakikishia ushindi klabu hiyo ya London.

Lakini pia unaweza ukaweka machaguo zaidi ya 1000 kwenye mtanange huu wa leo ambapo hapo utakuwa na nafasi ya kushinda kabisa, lakini pia unaweza ukatumia BET BUILDER kufanya ubashiri mechi hii.

LALIGA kule Hispania pia itaendelea kwa michezo kadhaa lakini sisi tutajikita kwenye mechi ya Barcelona dhidi ya Rayo Vallecano ambapo mabingwa hao watetezi wanataka kuanza msimu wakiwa na kasi nzuri katika harakati za kutetea ubingwa wao.

Chini ya Hansi Flick wanaingia kwenye mchezo wakiwa na kikosi chenye uwezo mkubwa wa kutawala mpira. Mfumo wao unategemea pasi za haraka, pressing baada ya kupoteza mpira na kutumia kasi ya wachezaji wa pembeni.

Kitu muhimu zaidi kitakuwa kufungua ulinzi wa Rayo, kwa sababu Rayo si timu rahisi. Barca wanahitaji kufanya kazi ya ziada kuhakikisha wanafungua nafasi za kalbu hiyo na kuweza kupata magoli. Beti hapa.

Barcelona wanahitaji kuzungusha mpira kwa haraka na kutumia nafasi kati ya mabeki na viungo wa Rayo.

Lakini pia mchezo huu pia unaweza kuwa muhimu kwa Rodri, ambaye anatarajiwa kupata dakika zake za kwanza Barcelona baada ya kujiunga kutoka Manchester City. Flick amesema anatarajiwa kucheza dakika chache na uzoefu wake unaweza kusaidia Barcelona kuongeza udhibiti wa kiungo.

Je pesa yako unaiweka kwa nani kati ya hizi timu mbili?. Ingia kwenye akaunti yako na usuka jamvi la ushindi siku ya leo.
Na Mwandishi Wetu

MTAALAM katika Sekta ya Mafuta nchini Dkt Sajad Habib Rai amempongeza Makamu wa Rais Ndejembi kwa kuapishwa kwake kushika nafasi hiyo huku akisisitiza hana shaka na uwezo na uadilifu wake katika kulitumikia Taifa la Tanzania akimsaidia Rais Samia Suluhu Hassan

Akizungumza jijini Dar es Salaam siku moja baada ya uapisho wa Makamu Rais huyo Ikulu ya Cha Chamwino, Dodoma, Dkt Sajad amesema ana imani kubwa na Kiongozi huyo huku akimpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa uteuzi wa Ndejembi.

Dkt Sajad ambaye ni Meneja Mkazi wa Mansoor Industries nchini, amesema hana shaka na uwezo wa Ndejembi katika uongozi akisisitiza kwa sifa na uwezo alionao ni msaada tosha katika usaidizi kwa Dkt Samia Suluhu Hassan.

" Kwa kipindi kifupi alichohudumu katika Wizara ya Nishati kwa nafasi ya Uwaziri , Mheshimiwa Ndejembi amekuwa mtu muhimu aliyesimama kikamilifu katika kuahughulikia masuala mbalimbali, hii ni sifa ambayo siyo kila Kiongozi anayo" amesema Dkt Sajad

Amesema hatua ya Rais Samia Hassan kumteua na baadae jina lake kupitishwa na Bunge, kunatokana uwezo wake hatua iliyomfanya kiongozi huyo Mkuu wa nchi kujenga imani dhidi yake hivyo anapaswa kuendelea kumuonesha imani hiyo wakati huu anapomsaidia katika majukumu makubwa zaidi Kiongozi.

Mtaalamu huyo wa Nishati pamoja na Mawasiliano aliyeisaidia Serikali katika 'upigaji mafuta' bandarini kupitia ubunifu wake wa mfumo maalumu wa udhibiti wa mafuta (BIL) amewataka wananchi kumuamini Ndejembi sambamba na kumpa ushirikiano wakati huu anapotekeleza wajibu wake.

Pamoja na wananchi Dkt Sajad pia amewataka watendaji wote wa Serikali, Wabunge pamoja na wafanyabiashara nchini wakiwemo waliomo katika sekta ya mafuta kuendelea kumuunga mkono Makamu wa Rais Ndejembi ili aweze kutimiza kikamilifu majukumu yake ya kumsaidia Rais Samia na Taifa kwa ujumla.

Ndejembi ambaye amehudumu katika nafasi mbalimbali za utumishi pamoja na uongozi ikiwemo ya Waziri wa Utumishi baadae Waziri wa Nishati ameapishwa jana kushika nafasi hiyo ya Makamu wa Rais baada ya mtangulizi wake Dkt Emmanuel Nchimbi kujiuzuru hivi karibuni.



Na Mwandishi Wetu
SERIKALI imezitaka shule nchini kuweka kipaumbele kwenye mafunzo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kwa wanafunzi wao ili kwenda sanjari na dunia ya sasa ya utandawazi na teknolojia inayokua kwa kasi. Imesema teknolojia inakwenda kwa kasi kubwa hivyo shule zinapaswa kuwa na miundombinu bora ya wanafunzi kujifunza TEHAMA, huku ikiipongeza shule ya Bunazi Green Acres iliyoko mji mdogo wa Bunazi, Kata ya Kassambya, wilayani Missenyi, kwa kuwa mfano kwenye eneo la mafunzo ya TEHAMA.

Ushauri huo ulitolewa mwishoni mwa wiki na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Missenyi mkoani Kagera, Phocus Rwegasira, wakati wa mahafali ya 10 ya shule hiyo yaliyofanyika shuleni hapo, ambapo alikuwa mgeni rasmi. Alisisitiza kuwa mafunzo ya teknolojia ni muhimu kwani dunia inakwenda kwa kasi kwenye eneo hilo, huku akisisitiza pia umuhimu wa ushirikiano kati ya wazazi, walimu na jamii katika kuhakikisha watoto wanapata elimu bora na malezi yanayowaandaa kuwa viongozi na wataalamu wa baadaye.

Alisema pamoja na shule hiyo kuweka miundombinu bora na ya kisasa, mafanikio ya mwanafunzi hayawezi kutenganishwa na juhudi za walimu, wazazi na uongozi wa shule, hivyo kila upande unapaswa kutekeleza wajibu wake kwa umakini. Rwegasira pia aliwahimiza wahitimu kuwa na nidhamu, bidii na kujituma katika masomo yao ya ngazi zinazofuata, akiwataka kutumia fursa za elimu kujenga maisha yao na kuchangia maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.

Aidha, aliwataka wazazi kuendelea kuwa karibu na watoto wao, kufuatilia maendeleo yao ya kitaaluma na kuwajengea misingi mizuri ya maadili. Katika hafla hiyo, Rwegasira alikabidhi vyeti kwa baadhi ya wahitimu, huku akipongeza uongozi wa Bunazi Green Acres kwa kutimiza miaka 10 ya mahafali na kuendelea kutoa mchango katika sekta ya elimu nchini.

Mkurugenzi wa Shule ya Bunazi Green Acres, Jackline Rushaigo, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya shule, wazazi na jamii katika kuhakikisha wanafunzi wanapata elimu bora na malezi yenye misingi ya maadili. Alisema mafanikio yaliyofikiwa na shule hiyo ni matokeo ya juhudi za pamoja za walimu, wazazi, wanafunzi na wadau wa elimu, huku akiwapongeza wanafunzi waliohitimu kwa hatua waliyofikia na kuwataka kuendelea kuwa na nidhamu, bidii na kujituma katika masomo yao ya ngazi zinazofuata.

Aidha, aliwashukuru wazazi na walezi kwa kuendelea kuiamini shule hiyo na kushirikiana na uongozi katika kuhakikisha wanafunzi wanapata mazingira bora ya kujifunza na kukua kitaaluma na kimaadili.

Mkuu wa shule hiyo, Geoffrey Moses, alisema shule hiyo tangu kuanzishwa kwake miaka 10 iliyopita imepata mafanikio makubwa kwani wanafunzi wake wote wamekuwa wakipata daraja A katika matokeo ya mitihani ya kitaifa inayotangazwa na Baraza la Taifa la Mitihani (NECTA). Alisema shule imejitahidi kuboresha miundombinu yake kwa kujenga majengo sita ya madarasa yenye vyumba 25 vya kujifunzia na imejenga maabara ya kisasa ya TEHAMA yenye huduma za mtandao kwa ajili ya mafunzo kwa vitendo.

Alisema shule imejitahidi kujenga maktaba yenye vitabu vingi vya kiada na vya ziada na mabweni sita yenye vitanda kwa kila mwanafunzi, na kwamba mazingira hayo ndiyo yameiwezesha shule kutoa huduma bora na matokeo mazuri kila mwaka. “Tunajivunia kwamba miaka yote 10 tangu shule ianze tumefanya vizuri kitaaluma, tumeshatoa wanafunzi 500 kwa miaka yote 10 na muda wote huo shule imekuwa ikipata wastani wa alama 251 ambayo ni daraja A bora,” alisema.

Aidha, alisema mafanikio ya shule hiyo yametokana na juhudi kubwa za walimu wake, nidhamu ya wanafunzi na ushirikiano mkubwa wa wazazi na serikali kuanzia ngazi ya kata hadi ngazi ya Wizara. “Mwaka huu tuna wahitimu 64 wa darasa la saba ambao tunaamini wataendeleza historia yetu nzuri ya kitaaluma kwa sababu wameandaliwa vizuri sana,” alisema.

Aidha, Mkuu huyo wa shule alisema katika kutambua ulimwengu unavyokwenda kwa kasi kwenye teknolojia, shule imeanzisha maabara ya TEHAMA yenye mtandao ili kuwapa wanafunzi ujuzi wa kompyuta kwa vitendo. “Wanafunzi wetu wanajivunia kutumia teknolojia kwa kujiamini na kwa ubunifu, hivyo tunaamini ujuzi huu utawaandaa kushindana na kufanikiwa katika dunia ya sasa,” alisema mwalimu Moses.




Top News