Na. Mwandishi wetu, DODOMA


Wizara ya Afya kupitia Idara ya Kinga, Sehemu ya Elimu ya Afya kwa Umma, imewataka wananchi wa Jiji la Dodoma kujitokeza na kuwapeleka watoto wenye umri wa chini ya miaka 10 kupata chanjo ya matone ya Polio, ikiwa ni sehemu ya kampeni ya kuongeza kinga dhidi ya ugonjwa huo.

Akizungumza kuhusu kampeni hiyo, Magdalena Dinawi kutoka Wizara ya Afya, Idara ya Kinga, alisema kuwa chanjo ya Polio inayotolewa kwa njia ya matone ni muhimu katika kuzuia ugonjwa wa kupooza unaosababishwa na virusi vya Polio.

Alisema kuwa ugonjwa huo hauna tiba, hivyo kinga kupitia chanjo ndiyo njia muhimu ya kumkinga mtoto dhidi ya madhara yanayoweza kusababishwa na Polio.

“Chanjo hii ina umuhimu kwa watoto kwa sababu inazuia ugonjwa wa kupooza ambao kitaalamu tunauita Polio. Ugonjwa wa Polio hauna tiba, ila kinga iliyopo ni kwa kupewa matone ya chanjo ya Polio. Aidha, watoto wanatarajiwa kupata huduma hiyo katika vituo vya kutolea huduma za afya, shule, maeneo ya ibada, masoko, magulio na maeneo mengine ambako watoto wenye umri wa chini ya miaka 10 wanapatikana,” alisema Dinawi.

Aliongeza kuwa katika kuhakikisha kampeni hiyo inawafikia watoto wengi, wizara imewashirikisha watu maarufu, viongozi wa dini, wazee wa mila na watu mashuhuri katika Jiji la Dodoma ili kusaidia kuhamasisha jamii kuwapeleka watoto kupata chanjo.

Kwa upande wake, Mratibu wa Huduma za Chanjo wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Victor Kweka alisema kuwa halmashauri hiyo imelenga kuwafikia jumla ya watoto 207,096 wenye umri wa chini ya miaka 10 katika kampeni hiyo.

Aliongeza kuwa halmashauri imeweka mikakati mbalimbali kuhakikisha hakuna mtoto anayekosa chanjo, ikiwemo kutembelea shule zote za awali na msingi pamoja na kufanya kampeni ya nyumba kwa nyumba.

“Tutahakikisha tunapita nyumba kwa nyumba ili kuhakikisha hatuachi mtoto yeyote bila kumpatia chanjo. Tunafahamu kwamba wakati mwingine watoto wanaweza wasiwe shuleni au wasiwe nyumbani,” alisema Kweka.

Aliongeza kuwa timu maalumu zitaelekezwa katika maeneo yenye mkusanyiko wa watu, ikiwemo masoko na vituo vya mabasi, ili kuwafikia watoto ambao huenda wasipatikane shuleni au nyumbani wakati wa utoaji wa chanjo.

Akizungumza katika semina hiyo ya uhamasishaji, mmoja wa viongozi wa dini, Shekh Ahmed Said alishukuru kwa semina hiyo, akiahidi kushirikiana na viongozi wengine wa dini kuhakikisha ujumbe kuhusu umuhimu wa chanjo unawafikia waumini na jamii kwa ujumla.

Wizara ya Afya na Halmashauri ya Jiji la Dodoma zimeendelea kuwahimiza wazazi, walezi na jamii kwa ujumla kutumia fursa hiyo kuwapeleka watoto wenye umri wa chini ya miaka 10 kupata chanjo ya matone ya Polio ili kuongeza kinga kwa watoto, familia, jamii na taifa kwa ujumla.










Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu imeiomba Serikali kuongeza ruzuku kwa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), ili kuwezesha kuongeza kasi ya ujenzi wa nyumba za makazi ya watumishi wa umma nchini.

Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Selemani Kakoso, wakati wa ziara ya kukagua miradi ya nyumba za watumishi inayotekelezwa na TBA katika maeneo ya Kisasa na Nzuguni jijini Dodoma, ikiwa ni sehemu ya ziara ya kutathmini utekelezaji wa miradi ya miundombinu nchini.

Kakoso amesema Kamati imejiridhisha na juhudi zinazofanywa na Serikali pamoja na TBA katika kukabiliana na changamoto ya makazi kwa watumishi wa umma, huku akisisitiza umuhimu wa kuongeza kasi ya ujenzi kutokana na mahitaji makubwa ya nyumba nchini.

Amesema eneo la Nzuguni lenye takribani ekari 630 lililotengwa kwa ajili ya ujenzi wa makazi ni hatua muhimu katika kuendeleza mji mpya wa Serikali, kwa kuwa uwepo wa nyumba hizo utawasaidia watumishi, wakiwemo walio katika ngazi za chini, kupata makazi yaliyo karibu na maeneo yao ya kazi.

“Tunawapongeza Serikali kwa juhudi kubwa zilizofanyika na pia TBA kwa mipango mizuri ya kuandaa nyumba za makazi ya watumishi. Tumekagua eneo la Kisasa na tumeona maboresho makubwa katika nyumba zilizojengwa,” amesema Kakoso.

Hata hivyo, Kamati imeishauri Serikali kuharakisha upatikanaji wa wabia kupitia utaratibu wa Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP), ili kuongeza uwezo wa TBA kutekeleza miradi mikubwa ya nyumba kwa wakati na kukidhi mahitaji ya watumishi.

Kwa mujibu wa Kamati hiyo, ushirikishwaji wa sekta binafsi utawezesha kupatikana kwa mitaji na utaalamu zaidi, huku Serikali ikiendelea kusimamia miradi hiyo kuhakikisha inatoa huduma bora na nyumba zenye viwango vinavyokidhi mahitaji ya watumishi.

Kuhusu huduma ya maji, Kamati imepongeza TBA kwa kuanzisha mfumo wake wa maji bila kutegemea kikamilifu huduma kutoka Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dodoma (DUWASA).

Hata hivyo, imeitaka TBA kuongeza juhudi za kuchimba visima na kuimarisha mifumo ya majitaka ili kukidhi mahitaji ya eneo hilo kwa muda mrefu.

Aidha, Kamati imeishauri TBA kuangalia uwezekano wa kutumia nishati ya jua kama chanzo mbadala cha umeme, hatua ambayo itasaidia kupunguza utegemezi wa mfumo wa kawaida wa umeme na kuhakikisha huduma zinaendelea kupatikana wakati changamoto za umeme zinapotokea.

Vilevile, Kamati imeitaka Wizara ya Ujenzi kushirikiana na Ofisi ya Rais-TAMISEMI, TANROADS, TARURA pamoja na TBA katika ujenzi wa miundombinu bora ya barabara katika maeneo hayo, hususan barabara za lami, ili kuongeza mvuto wa makazi hayo na kurahisisha usafiri.

Kamati imesisitiza kuwa ujenzi wa nyumba za watumishi ni uwekezaji wa muda mrefu unaopaswa kuzingatia thamani ya fedha, ubora wa majengo na mahitaji ya wananchi, ili miundombinu hiyo iwe na tija kwa Serikali na kizazi cha sasa na kijacho.

Naye Mkurugenzi wa Idara ya Miliki wa TBA, Said Rajabu Mndeme, aliyemwakilisha Mtendaji Mkuu wa TBA, amesema mradi huo unatekelezwa katika eneo lenye takribani ekari 640, ambapo ujenzi wa nyumba 150 tayari umekamilika.

Amesema nyumba nyingine 110 zipo katika hatua mbalimbali za ujenzi, zikiwemo nyumba 50 za chini zilizofikia hatua ya mwisho na zinatarajiwa kuanza kutumika. Aidha, majengo mawili ya ghorofa tano yako katika hatua ya msingi, ambapo kila jengo litakuwa na uwezo wa kuhudumia familia 30.

Kwa mujibu wa Mndeme, TBA imeanza kushirikisha sekta binafsi katika utekelezaji wa mradi huo baada ya eneo hilo kutangazwa na wadau mbalimbali wa ndani na nje ya nchi kuwasilisha mapendekezo ya kushirikiana na Wakala.

Amesema mradi huo umepangwa kuwa na huduma muhimu zikiwemo shule za awali, shule mbili za msingi, maeneo ya biashara pamoja na vyuo.

Mndeme amesema mahitaji ya nyumba katika Jiji la Dodoma ni makubwa, akifichua kuwa wakati ujenzi wa nyumba 150 za awali ulipokuwa ukiendelea, TBA ilipokea zaidi ya maombi 1,000 kutoka kwa watumishi waliokuwa wakihitaji makazi.

Amesema hadi sasa, Meneja wa TBA Mkoa wa Dodoma ana maombi zaidi ya 8,000 ya nyumba kutoka kwa watumishi na wananchi, hali inayoonyesha ukubwa wa changamoto ya makazi katika jiji hilo.

Mndeme ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita na Wizara ya Ujenzi kwa kuendelea kuiwezesha TBA kupitia ruzuku, akisema mradi huo ulioanza mwaka 2021 umeendelea kutekelezwa kwa ufadhili wa Serikali.

Amesema TBA sasa inalenga kuongeza kasi ya ushirikishwaji wa sekta binafsi ili kuharakisha ukamilishaji wa mpango wa ujenzi wa nyumba 3,500 na hivyo kupunguza changamoto ya makazi katika Jiji la Dodoma.



Na Oscar Assenga, TANGA

Programu ya Tanga Yetu imeendelea kuwa chachu ya maendeleo kwa vijana na watoto wa Jiji la Tanga, kupitia miradi inayolenga kuimarisha elimu, ujuzi, teknolojia na ubunifu kwa ajili ya kutatua changamoto mbalimbali zinazoikabili jamii.

Akizungumza katika Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu, Afisa Mawasiliano wa Programu ya Tanga Yetu, Cliford Sangai, alisema programu hiyo inayofadhiliwa na Foundation Botnar na kutekelezwa na Kampuni ya Innovate kwa kushirikiana na Halmashauri ya Jiji la Tanga, imeshiriki maonyesho hayo kuonyesha matokeo ya miradi mbalimbali inayotekelezwa jijini humo.

Alisema Tanga Yetu inatekeleza zaidi ya miradi 15 katika maeneo ya elimu, teknolojia na ubunifu, ikiwa na lengo la kuhakikisha watoto na vijana wanapata fursa za kukuza uwezo wao na kutumia maarifa kutatua changamoto zinazowakabili.


“Tumekuja kwenye wiki hii kuonyesha namna ambavyo Tanga Yetu imekuwa ikifadhili miradi mbalimbali katika elimu, ujuzi na ubunifu, pamoja na kuonyesha bidhaa na suluhisho zinazotokana na mawazo ya vijana wa Tanga,” alisema Sangai.

Kwa mujibu wa Sangai, baadhi ya miradi inayotekelezwa inalenga kukabiliana na changamoto ya watoto katika kujifunza kusoma na kuandika, huku matokeo ya mradi huo yakitumika katika kutengeneza mpango wa Kitaifa wa KKK.

Alisema programu hiyo pia imejikita katika kuwawezesha vijana kutumia vipaji na ujuzi wao katika teknolojia na ubunifu, akisisitiza kuwa vijana wa Tanga wana uwezo wa kubuni na kutengeneza bidhaa zinazoweza kutatua changamoto za jamii na hata kufikia soko la kitaifa.

“Vitu ambavyo tunaona vinafanyika katika miji mingine vinafanyika pia Tanga. Vijana wetu wamekuja na bidhaa walizobuni na kuzitengeneza wenyewe, jambo linaloonyesha uwezo mkubwa walionao,” alisema.

Sangai alisema katika eneo la ujuzi, Tanga Yetu imekuwa ikiwawezesha vijana kupata mafunzo mbalimbali yanayowaongezea uwezo wa kujiajiri na kuzalisha kipato kupitia teknolojia.

Alitaja baadhi ya mafunzo hayo kuwa ni Graphic Design, uchapishaji wa mabango na T-shirt, utengenezaji wa maudhui ya kidijitali (Content Creation), usimamizi wa mitandao ya kijamii (Social Media Management) pamoja na ujuzi mwingine wa kidijitali.

Alisema vijana wanaotembelea banda la Tanga Yetu katika maonyesho hayo wanaweza kuona miradi mbalimbali inayotekelezwa katika maeneo ya elimu, ujuzi na ubunifu, pamoja na namna inavyowasaidia vijana wa Tanga kujenga uwezo na kutengeneza fursa.



Sangai alisema Tanga Yetu pia imeanzisha Mfuko wa Ubunifu wa Tanga Yetu, ambao umewezesha vijana wanane kupata ufadhili wa kujaribu mawazo yao ya kibunifu yenye lengo la kutatua changamoto zinazoikabili jamii ya Jiji la Tanga.

Alisema miongoni mwa miradi hiyo ni mfumo unaolenga kuwasaidia wavuvi kufahamu maeneo yenye samaki pamoja na kufuatilia usalama wa vyombo vyao wanapokuwa baharini.

“Tumeshazoea wavuvi kuamka usiku na kwenda kuvua bila kujua samaki wapo wapi. Vijana wamekuja na mfumo unaoweza kumsaidia mvuvi kufahamu eneo ambalo samaki wapo na kwenda kuvua kwa ufanisi zaidi,” alisema.

Aliongeza kuwa mfumo huo pia unafuatilia mwenendo wa chombo cha uvuvi, hivyo iwapo kunapotokea ajali baharini, watu waliopo nchi kavu wanaweza kufahamu eneo ambalo chombo hicho kimepata tatizo na kuchukua hatua kwa haraka.

Sangai alisema hatua hiyo inaonyesha namna ubunifu unavyoweza kutumika kama nyenzo ya kutatua changamoto zinazolikabili Jiji la Tanga na Taifa kwa ujumla.


Kwa upande wake, Zainabu Msuya, mnufaika wa Mradi wa Kidijitali unaosimamiwa na Swahili Digital chini ya Programu ya Tanga Yetu, alisema amepata fursa ya kujifunza ujuzi mbalimbali wa teknolojia na sasa anaweza kutumia maarifa hayo kujiajiri na kuwawezesha vijana wengine.

Alisema mradi huo unatoa mafunzo katika maeneo ya Graphic Design, Artificial Intelligence (AI), Content Creation, Social Media Management na ujuzi wa kidijitali kwa ujumla.

Msuya alisema yeye ni mmoja wa wanufaika wa awamu ya kwanza ya mafunzo hayo na baadaye alipata nafasi ya kuwa mmoja wa wasimamizi katika awamu zilizofuata.

“Mradi huu umeweza kuwawezesha vijana wengi. Kwa awamu zilizofuata tulihusisha vijana 100 kwa kila awamu, na kwa ujumla vijana 300 wamepata mafunzo kupitia programu hii,” alisema.

Alisema mafunzo hayo yamewasaidia vijana kuongeza uelewa wa teknolojia na kupata uwezo wa kutumia mitandao ya kijamii kama sehemu ya kujenga fursa za kiuchumi.

Naye Swahibu Bilal, msimamizi wa mradi wa kidijitali, alisema programu hiyo imekuwa ikiwafundisha vijana namna ya kutumia mitandao ya kijamii kwa ufanisi na kuitumia kama nyenzo ya kutengeneza kipato.

Alisema awali vijana wengi hawakuwa na uelewa wa kutosha kuhusu matumizi ya mitandao ya kijamii kibiashara, lakini kupitia mafunzo hayo wameweza kujifunza namna ya kusimamia akaunti, kutengeneza maudhui na kutumia majukwaa hayo kukuza shughuli zao.

“Vijana wengi awali walikuwa hawaelewi namna ya kutumia mitandao ya kijamii kutengeneza kipato, lakini kupitia mafunzo haya sasa wanaweza kufanya mambo mbalimbali na kutumia ujuzi huo kujenga fursa zao,” alisema Bilal.

Programu ya Tanga Yetu inaendelea kushirikisha vijana katika elimu, ujuzi, teknolojia na ubunifu, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuwaandaa kutumia maarifa na vipaji vyao katika kutatua changamoto za jamii na kuchangia maendeleo ya Jiji la Tanga na Taifa kwa ujumla.




Mameneja wa Kanda na Mikoa wa Taasisi za Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Tume ya Ushindani (FCC) pamoja na Wakala wa Vipimo Tanzania (WMA) wameagizwa kuhakikisha hakuna bidhaa bandia na duni katika maeneo yao wanayoyasimamia kiutendaji.

Maelekezo hayo yametolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Mhe. Balozi Waziri Rajab Salum, wakati wa kikao cha menejimenti za Tume ya Ushindani (FCC), Shirika la Viwango Tanzania (TBS) pamoja na Wakala wa Vipimo Tanzania (WMA), Agosti 21, 2026 jijini Dodoma, kwa lengo la kujadili na kupanga mikakati ya kuimarisha udhibiti wa bidhaa bandia nchini.

Katika kikao hicho, Balozi Salum amesisitiza umuhimu wa taasisi hizo kufanya kazi kwa ushirikiano, weledi, haki na uwajibikaji, akieleza kuwa uratibu mzuri ni muhimu katika kuhakikisha bidhaa zisizokidhi viwango na bidhaa bandia hazitawali soko.

Amesema udhibiti wa bidhaa bandia ni suala muhimu katika kulinda mlaji, wafanyabiashara wanaofuata sheria pamoja na uchumi wa nchi, hivyo taasisi zenye dhamana ya kusimamia soko zinapaswa kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na kwa kuzingatia sheria na taratibu zilizowekwa.

Balozi Salum amezitaka FCC, TBS na WMA kuongeza ushirikiano katika kubadilishana taarifa, kufanya ukaguzi na kuchukua hatua stahiki dhidi ya wanaojihusisha na uzalishaji, uingizaji au usambazaji wa bidhaa bandia na zisizokidhi viwango.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa watumishi wa taasisi hizo kuwa waadilifu na kutekeleza majukumu yao kwa haki, ili kuhakikisha wafanyabiashara wanafuata sheria wanapata mazingira sawa ya ushindani na walaji wanapata bidhaa salama na zenye ubora.

Amesema matumizi ya teknolojia na taarifa sahihi yanapaswa kupewa kipaumbele katika kuimarisha mifumo ya udhibiti, kutokana na mabadiliko ya mbinu zinazotumiwa na baadhi ya watu katika kusambaza bidhaa bandia katika masoko.

Kwa upande mwingine, kikao hicho kimekuwa fursa kwa viongozi wa FCC, TBS na WMA kueleza changamoto zinazowakabili katika utekelezaji wa majukumu yao, pamoja na kuweka mikakati ya pamoja ya kuongeza ufanisi katika usimamizi wa soko.

Balozi Salum amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi zake ili kujenga mazingira ya biashara yenye ushindani wa haki, kulinda walaji na kuhakikisha wafanyabiashara wanaofuata sheria wanaendelea kufanya shughuli zao katika mazingira salama na yenye tija.

Kikao hicho ni sehemu ya jitihada za Wizara ya Viwanda na Biashara kuimarisha uratibu wa taasisi zake na kuhakikisha majukumu ya udhibiti wa soko yanatekelezwa kwa weledi, haki, uwajibikaji na kwa kuzingatia maslahi mapana ya Taifa.









Top News