NA DENIS MLOWE, IRINGA 

MWENYEKITI wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji (Rufaa) Jacobs Mwambegele, leo amefungua rasmi mafunzo ya siku tatu kwa watendaji wa uchaguzi ngazi ya mkoa, jimbo na kata yanayofanyika mkoani Iringa, akisisitiza uadilifu, weledi na uzingatiaji wa sheria katika mchakato wa uchaguzi.

Akizungumza mbele ya waratibu wa uchaguzi wa mikoa, wasimamizi wa uchaguzi, wasimamizi wasaidizi, maafisa uchaguzi, wahasibu, maafisa ununuzi na wanahabari, Mhe. Mwambegele alianza kwa kuwatakia washiriki heri ya mwaka mpya 2026 na kuwapongeza kwa kuteuliwa kutekeleza jukumu muhimu la kusimamia uchaguzi mdogo wa Ubunge Jimbo la Peramiho na Udiwani Kata ya Shiwinga.

Mwenyekiti huyo alieleza kuwa uteuzi wa watendaji hao umezingatia matakwa ya Sheria ya Uchaguzi ya mwaka 2024, ikiwemo sifa za uadilifu, weledi na uzoefu katika masuala ya uchaguzi. “Ni muhimu kuheshimu viapo vyenu na kutekeleza majukumu kwa kuzingatia Katiba, sheria za uchaguzi, kanuni na maelekezo ya Tume,” alisisitiza

Katika hotuba yake, Mhe. Mwambegele aliwakumbusha washiriki kuwa uchaguzi ni mchakato wenye hatua nyingi za kisheria zinazotakiwa kufuatwa kwa umakini ili kuepusha malalamiko na vurugu. Alionya dhidi ya kufanya kazi kwa mazoea kwa sababu  kila uchaguzi unatofautiana na mwingine.

Aidha, aliwataka watendaji kuwa karibu na vyama vya siasa vyenye usajili kamili na wadau wengine ili kuongeza uwazi, uaminifu na urahisi wa utekelezaji wa majukumu.

Katika mafunzo hayo, Mwenyekiti alibainisha masuala mahimu ambayo washiriki wanapaswa kuyazingatia, ikiwemo:

Kufanya utambuzi wa vituo vya kupigia kura mapema ili kubaini mahitaji na changamoto za miundombinu.

Kuhakikisha waajiriwa wa vituo vya kura ni wenye weledi na si watu waliopendekezwa kwa upendeleo, kuhakiki vifaa vya uchaguzi na kuhakikisha kila kituo kinafikiwa mapema.

Kuwapatia vyama vya siasa orodha ya vituo vya kupigia kura kwa maandalizi ya mawakala na kuhakikisha vituo vyote vinafunguliwa saa 1:00 asubuhi siku ya uchaguzi na kufanya mawasiliano ya karibu na Tume pale panapohitajika ushauri.

Mhe. Mwambegele pia aliwasihi washiriki kujifunza kwa makini, kushirikishana uzoefu na kuacha tabia ya kufanya kazi kwa mazoea, akisema maarifa na umakini ni msingi wa uchaguzi wenye ufanisi.

Baada ya kutoa maelekezo na maonyo muhimu, Mwenyekiti huyo alitangaza rasmi kufunguliwa kwa mafunzo ya siku tatu yatakayofanyika kuanzia Januari 24 hadi 26, 2026.

“Ni matarajio ya Tume kwamba kila mmoja atatoka hapa akiwa na ujuzi wa kutosha wa kusimamia uchaguzi huu mdogo kwa ufanisi,” alisema kabla ya kumaliza hotuba yake na kuwashukuru washiriki wote.Baadhi ya wasimamizi waliopata mafunzo walisema kuwa mafunzo hayo yawasaidia kusimamia vyema chaguzi ndogo za marudio.

Mmoja wa Wasimamizi hao kutoka jimbo la Peramiho,  Salum Kateule alisema kuwa mafunzo yaliyoandaliwa na Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi kwa ajili ya uchaguzi mdogo wa Jimbo la Peramiho, mkoa wa Ruvuma. Uchaguzi huu umeitishwa kutokana na kifo cha aliyekuwa Mbunge, Mheshimiwa Jenista Mhagama.

 Leo tumekutana kwa ajili ya mafunzo ya watendaji ngazi ya mkoa, watendaji ngazi ya jimbo na ngazi ya kata. Mafunzo haya yamefunguliwa na Mheshimiwa Mwenyekiti, ambaye ametukumbusha kusimamia vyema majukumu yetu ya usimamizi wa uchaguzi mdogo wa Jimbo la Peramiho kulingana na sheria, katiba na kanuni za uchaguzi za mwaka 2016.

Wito wangu kwa wananchi wa Jimbo la Peramiho ni kwamba, kwanza, wajitokeze kuchukua fomu za kugombea. Kwa wale watakaoteuliwa, waendelee kuwasilisha sera na mipango ya vyama vyao kwa ajili ya kujinadi na kupata fursa ya kuteuliwa na wananchi.

Pili, nawaomba wananchi wa Jimbo la Peramiho kujitokeza kwa wingi wakati wa kampeni za uchaguzi, kuwasikiliza wagombea wote na kuwapa fursa sawa za kuwasikiliza.

Kateule aliwasihi wananchi wajitokeze siku ya kupiga kura ili kumchagua kiongozi ambaye wanamuona anafaa kuwatumikia na kuuwakilisha vyema Jimbo la Peramiho.

Naye Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la la mbozi, Dan Tweve, amesema maandalizi ya uchaguzi mdogo katika Kata ya Shiwinga yanaendelea vizuri kufuatia kifo cha diwani aliyeshinda kabla ya kuapishwa. 

Tweve amesema jukumu la wasimamizi ni kuhakikisha maandalizi ya msingi yanafanyika kwa ufanisi, ikiwemo kuwawezesha wagombea kuchukua fomu, kufanya kampeni kwa amani na hatimaye kuhakikisha uchaguzi unafanyika kwa haki na utulivu. 

Aidha, amesisitiza kuwa wapiga kura wote, wakiwemo watu wenye ulemavu, watapatiwa huduma na msaada unaohitajika ili washiriki bila vikwazo. Uchaguzi huo unatarajiwa kufanyika tarehe 26 Februari.










Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limetoa elimu kwa wananchi wa Mkoa wa Dodoma kuhusu madhara ya matumizi holela ya pombe, likilenga kuzuia athari za kiafya na kiuchumi zinazoweza kuwakumba wananchi na familia zao.

Elimu hiyo imetolewa kama sehemu ya jitihada za TBS za kuwafikia wananchi moja kwa moja na kuimarisha ulinzi wa afya ya jamii kwa kupunguza tatizo la uraibu wa unywaji pombe pamoja na magonjwa yanayotokana na matumizi yasiyo salama ya pombe.

Aidha, wananchi wamehamasishwa kutumia pombe zilizosajiliwa na zinazokidhi matakwa ya viwango vya ubora na usalama ili kujilinda dhidi ya bidhaa hatarishi zisizokidhi viwango.

TBS imeeleza kuwa itaendelea kutoa elimu kwa umma katika mikoa mbalimbali nchini ili kuhakikisha wananchi wanapata uelewa wa kutosha kuhusu matumizi salama ya bidhaa na huduma zinazopatikana sokoni.



Na Mwandishi wetu.

Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia taasisi zake inaendelea kunadi vivutio vya utalii vilivyopo Tanzania katika maonesho ya FITUR yanayoendelea nchini Hispania ambapo watu mbalimbali wakiwemo wananchi waliotembelea banda la Tanzania wameonekana kufurahishwa zaidi na tukio la kuzaliana na kuhama kwa nyumbu kutoka hifadhi moja kwenda nyingine (The Great Wildebeest Migration).

Kamishna Msaidizi Mwandamizi anayesimamia Utalii na Masoko NCAA, Mariam Kobelo, ameelezea wageni wanaotembelea banda hilo kuhusu tukio hilo muhimu katika ikolojia na la kipekee duniani kwa namna nyumbu jike wanavyoshika mimba na kuzaa kwa wakati mmoja katika eneo la tambarare za Ndutu, Ngorongoro kuzaa na hatimaye kuendelea na safari yao kuelekea Serengeti.

Ameongeza kuwa tukio la kuzaliana kwa nyumbu huanza mwezi Desemba hadi Machi kila mwaka katika eneo la Ndutu Ngorongoro, eneo hili ni salama zaidi kiulinzi, malisho, maji, mandhari, hali ya hewa, na virutubishi vinavyowawezesha ndama kukua na kuchangamka kwa haraka na pia kuna uchache wa wanyama wakali ambao huhatarisha ustawi wa viumbe vinavyozaliwa.

 Vilevile, udongo wa eneo la Ndutu una madini asilia yanayochangia nyumbu jike kutoa maziwa yenye virutubisho vya kutosha kwa ajili ya kunyonyesha, huku yakisaidia pia ukuaji imara wa mifupa ya ndama katika hatua za awali za maisha yao, alisema Kamishna Msaidizi Mwandamizi Kobelo.

Sambamba na kuelezea tukio la kuzaliana kwa nyumbu, alielezea kuwa NCAA imeendelea kunadi vivutio vingine ambavyo havijulikani sana kama vile mlima Loolmalasin, Mapango ya tembo na maporomoko ya maji Endoro, Engaruka, Mumba Shelter Rocks, Kimondo cha Mbozi na Jiopaki ya Ngorongoro-Lengai kwa ujumla.

Katika maonesho hayo ujumbe wa Tanzania ulipata nafasi ya kuzungumza na Ofisa kutoka Ubalozi wa Tanzania nchini Ufaransa, Bi. Eva Mashala, ambaye amepongeza kazi kubwa inayofanywa na Wizara ya Maliasili na Utalii pamoja na taasisi zake katika kutangaza utalii nje ya nchi kupitia Maonesho mbalimbali na kuongeza chachukwa ongezeko la wageni na kukuza pato la Taifa. 

Pamoja naye Kamishna Kobelo ameambatana na Afisa Utalii Bw. Yohana Nkwamah.





 

NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara, Deniss Londo, amesema kupitia Shirika la Utafiti na Maendeleo ya Viwanda Tanzania (TIRDO),vijana wabunifu wanapata fursa ya kubadili mawazo yao ya kiteknolojia na ujasiriamali kuwa bidhaa na huduma zenye tija katika soko.

Amesema viwanda vina mchango mkubwa katika utoaji wa ajira, kuimarisha usalama wa kiuchumi na kukuza ubunifu, hususan kwa vijana.

Ameyasema hayo leo Januari 23, 2026 Jijini Dar es Salaam alipotembelea ofisi za TIRDO ambapo amefurahishwa na shughuli inayofanywa na shirika hilo hasa utafiti kwenye maendeleo ya viwanda nchini.

Amesema kuwa jukumu la TIRDO si kuanzisha viwanda moja kwa moja, bali ni kufanya utafiti, kusambaza teknolojia na kusaidia wazalishaji wadogo na wa kati kupunguza gharama za uzalishaji na kuongeza tija.

Aidha amewapongeza viongozi na wataalamu wa TIRDO kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kulea wajasiriamali waliotoka ngazi ya chini hadi kufikia uzalishaji wa viwandani ambapo kuvutiwa na miradi ya urejelezaji wa taka za plastiki pamoja na matumizi ya teknolojia rafiki kwa mazingira, akisema miradi hiyo inalinda mazingira na wakati huo huo kuleta ajira kwa wananchi.

Hata hivyo amesema kuwa ushirikiano kati ya wizara, taasisi za umma na mamlaka za serikali za mitaa ni muhimu ili kuhakikisha miradi ya viwanda inatekelezwa kwa kuzingatia sera, viwango na mahitaji halisi ya wananchi. Ameahidi kuyafikisha mapendekezo ya wadau katika ngazi ya wizara kwa lengo la kuyaendeleza katika maeneo mbalimbali nchini.

Pamoja na hayo amesema kuwa maendeleo ya viwanda bado ni nguzo kuu ya ukombozi wa kiuchumi wa Tanzania, akisisitiza kuwa bila uwekezaji wa kimkakati katika sekta ya viwanda, taifa haliwezi kufikia maendeleo endelevu.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TIRDO, Prof. Mkumbukwa Mtambo, amesema kuwa wanatarajia kuanzisha kituo cha kutengeneza na kufanyia matengenezo vifaa vya kielektroniki kwa ajili ya kukuza ubunifu wa ndani na kupunguza utegemezi wa teknolojia kutoka nje.



















Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Mhe. Edward Mpogolo, amefanikiwa kumaliza mgomo wa wafanyakazi zaidi ya 1,500 wa Kiwanda cha NAMERA kilichopo Gongolamboto, jijini Dar es Salaam, mgomo uliokuwa umeanza tarehe 16 Januari, 2026.

Mgomo huo ulitokana na madai ya mishahara, ambapo mshahara wa kima cha chini kwa sekta binafsi umewekwa kwa mujibu wa Tangazo na Amri ya Serikali Namba 605A ya tarehe 13 Oktoba, 2025, inayotoa ongezeko la wastani wa asilimia 33.4. 

Kutokana na ongezeko hilo, mshahara wa chini umeongezeka kutoka Shilingi 275,060 mwaka 2022 hadi Shilingi 358,222 mwaka 2025. Hivyo basi, hakuna mtu au taasisi yoyote inayoruhusiwa kulipa mshahara chini ya kiwango kilichobainishwa katika Amri hiyo ya Serikali, hata kwa kuwepo kwa makubaliano yoyote kati ya taasisi binafsi kupitia chama chao cha waajiri (ATE) au mifumo mingine ya ndani.
Akizungumza na wafanyakazi pamoja na uongozi wa kiwanda hicho, Mhe. Mpogolo amesisitiza kuwa Amri ya Serikali ni ya lazima kutekelezwa na kwamba hakuna kampuni, taasisi au mwajiri yeyote anayekubalika kushuka chini ya viwango vilivyowekwa kisheria. Ameeleza kuwa makubaliano yoyote hayawezi kwenda kinyume na Amri ya Serikali.
Mpogolo ametoa maelekezo muhimu kwa uongozi wa kiwanda na wafanyakazi, ikiwemo kuhakikisha malipo ya mishahara yanatolewa kwa mujibu wa Tangazo la Serikali Na. 605A la mwaka 2025, huku akisisitiza kuwa hakuna mfanyakazi atakayefukuzwa kutokana na kushiriki mgomo, ili kuimarisha mahusiano bora kati ya mwajiri na waajiriwa. 

Aidha, ameitaka kiwanda kushirikiana na Chama cha Wafanyakazi (TUICO) na Afisa Kazi wa Mkoa wa Dar es Salaam kufanyika uchaguzi wa viongozi wa wafanyakazi watakao kuwa kiungo madhubuti kati ya wafanyakazi na uongozi, pamoja na kupitia mikataba ya ajira kuhakikisha inakidhi sheria na kanuni zinazohitajika. Mpogolo pia amehimiza ujenzi wa mahusiano mazuri na kulinda kiwanda kutokana na mchango wake mkubwa katika uchumi wa taifa na nafasi zake muhimu za ajira kwa wananchi.

Kwa upande wao, wafanyakazi wa kiwanda hicho wameeleza kuridhishwa na hatua zilizochukuliwa na Mkuu wa Wilaya, wakisema kuwa zimeleta matumain

 


Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Dennis Londo amelipongeza Shirika la Maendeleo ya Viwanda Vidogo (SIDO) kwa kutekeleza ahadi ya siku 100 ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kutoa mikopo ya zaidi ya shilingi bilioni moja kwa wajasiriamali ili kuendeleza miradi mbalimbali ya viwanda nchini.

Amebainisha hayo Januari 23, 2026, alipofanya ziara ya kikazi katika shirika hilo na kuipongeza menejimenti kwa kasi ya kuridhisha ya utekelezaji wa maelekezo ya serikali.

Mhe. Londo amesisitiza kuwa viwanda vidogo ni moyo wa uchumi endelevu kwani vinamsaidia mwananchi hasa vijana kupata ajira na kuleta maendelwo kuanzia ngazi ya familia na kuchochea uingizaji wa fedha za kigeni.

Amesema kupitia SIDO, bidhaa za Kitanzania zinaweza kuteka soko kubwa la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), jambo litakaloinua hadhi ya viwanda vya ndani katika medani za kimataifa.

Kufuatia ziara hiyo, Naibu Waziri ameiagiza SIDO kuangalia namna ya kuongeza kutoa ruzuku (grants) kwa vijana ili kuhakikisha wanawekeza kwa kutumia rasilimali zilizopo bila kukwama, lengo ni kuhakikisha kuwa ukosefu wa mtaji haubaki kuwa kikwazo kwa vijana wabunifu wanaotaka kuingia katika sekta ya uzalishaji na viwanda.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Sera na Mipango, Bw. Audax Bahweitima, amesema Sera ya Maendeleo ya Wajasiriamali Wadogo na wa Kati (SMEs) inalenga kuboresha miundombinu ya biashara na teknolojia na kusisitiza kuwa SIDO ndiye mtekelezaji mkuu wa sera hiyo kwa kuhakikisha upatikanaji wa fedha na zana za kisasa za uzalishaji unawafikia walengwa kwa wakati.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa SIDO, Mhandisi Prof. Sylvester Mpanduji, amesema kuwa hadi sasa wanufaika 196 wamefikiwa na mikopo hiyo, na kufanikiwa kuzalisha jumla ya ajira 546. Takwimu hizo zinaonyesha mafanikio makubwa kwa kundi la vijana, ambao wamechukua nafasi 436 kati ya ajira hizo mpya zilizotengenezwa.

Aidha, Prof. Mpanduji ameongeza kuwa kupitia ushirikiano na Shirika la Kimataifa la Wahamiaji (IOM), wametoa ruzuku ya shilingi milioni 51 kwa vijana tisa ili kukuza viwanda vyao.















Top News