SERIKALI imejipanga kupeleka fedha kwenye miradi mbalimbali ya kimkakati ili wananchi waendelee kufaidika, ikiwemo kupata ajira katika sekta binafsi na serikalini.
‎Akizungumza Februari 26, 2026 wakati alipotembelea mradi wa ujenzi wa barabara ya Ntendo – Kizungu wenye urefu wa kilomita 25 kwa kiwango cha lami mkoani Rukwa, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu, amesema kuwa fedha zinazotolewa na Serikali zinalenga kuwanufaisha wananchi moja kwa moja kupitia fursa za ajira na kukuza kipato.
‎Ziara hiyo ni sehemu ya mwendelezo wa ukaguzi wa miradi ya maendeleo katika Mkoa wa Rukwa, ambapo Waziri Sangu alisisitiza kuwa dhamira ya Serikali ni kuhakikisha uwekezaji unaofanyika unaleta tija kwa wananchi wa maeneo husika.
‎Aidha, ametoa wito kwa mkandarasi wa mradi huo, China Geo Engineering Ltd, kuhakikisha kuwa ajira zinazohitaji wazawa zinatolewa kwa kipaumbele kwa wananchi wanaozunguka mradi huo ili waweze kunufaika moja kwa moja na utekelezaji wake.
‎Waziri Sangu amesema kuwa lengo la Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni kujenga uchumi imara, shindani na jumuishi unaowagusa wananchi wote.
‎“Tunaposema uchumi jumuishi ni kwamba fedha zinazokuja kwa wananchi ziweze kuzalisha ajira kwa wananchi wazawa,” amesema Waziri Sangu.
‎Katika hatua nyingine, ameitaka kampuni hiyo kuzingatia Sheria za Kazi katika utoaji wa ajira, ikiwemo kuhakikisha wafanyakazi wanaostahili wanapelekewa michango yao katika Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) pamoja na michango ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) kwa mujibu wa sheria.
‎Kaimu Meneja Wakala wa Barabara (TANROADS) Mkoa wa Rukwa Mhandisi Joseph Gimonge, amesema kuwa utekelezaji wa mradi unaendelea vizuri ambapo hadi sasa ujenzi umefikia asilimia 53.37.

‎Akizungumza kuhusu maendeleo ya mradi huo, Mha. Gimonge alieleza kuwa kazi zinaendelea kulingana na mpango uliopangwa, ambapo kwa hatua zilizofikiwa zinaendelea vizuri kulingana na maendeleo ya mradi.
‎Kwa upande wao, wananchi wa Kata ya Muze, Kijiji cha Kizungu, wameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa kupeleka fedha za ujenzi wa barabara hiyo katika awamu ya kwanza. Wamesema mradi huo umekuwa na manufaa makubwa kwao kwani umechangia kupatikana kwa ajira kwa wakazi wa eneo hilo pamoja na kukuza kipato chao.
‎Wananchi hao wameeleza kuwa kukamilika kwa barabara hiyo kutarahisisha usafirishaji na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika eneo lao.



*Ni baada ya kueleza kero yake kwa Waziri Mkuu
JITIHADA za Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba kusikiliza kero za wananchi zimezaa matunda ambapo mkazi wa Kata ya Baraa jijini Arusha, Bi. Agnes Simon Laizer alilipwa fidia ya sh. milioni 7 na mmiliki wa shule ya Nariva Hill (jirani yake) ambaye alikuwa ameharibu jiko na ukuta kutokana na ujenzi wa ghorofa unaoendelea.

Bi. Agnes alikabidhiwa fedha hizo taslimu jana (Alhamisi, Februari 26, 2026) mbele ya mwakilishi wa Katibu Tawala wa Mkoa, Bw. Polycarp Nkuyumba, Diwani wa Kata hiyo, Mtendaji wa Kata na Mtaa, pamoja na Maafisa wa Wilaya waliokuwa wameambatana na timu ya Wasaidizi wa Waziri Mkuu waliokuwa wakisikiliza kero za wananchi kama alivyoelekeza Waziri Mkuu.

Februari 24, mwaka huu, Bi. Agnes Laizer aliwasilisha kero yake mbele ya Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika eneo linapojengwa soko jipya la Kilombero wakati akiwa kwenye ziara ya siku tatu mkoani Arusha. Bi. Agnes alisema ameathirika kiafya kutokana na ujenzi wa ghorofa kwenye shule ya msingi ya Nariva ikiwemo kuharibiwa ukuta na kubomolewa jiko lake.

Alisema vumbi, zege, vipande vya matofali na mbao vinafika katika eneo lake (kwa kuwa hajaweka neti ya kuzuia), sehemu ya ghorofa imezidi katika eneo lake na bomba lake la maji ya kunywa lililochimbuliwa wakati ujenzi ukianza, bado halijafukiwa.

Februari 25, 2026 Bi. Agnes alifika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha ambako timu ya wataalamu wa Mkoa na Jiji walikutana na kusikiliza kero za wananchi na wakaamua kumuita mmiliki wa shule ya Nariva Hill, Bw. Emmanuel Saanya ambaye alikubali kulipa fidia kwa mama huyo.

Timu iliyofika nyumbani kwa Bi. Agnes Laizer ilishuhudia ujenzi wa ghorofa ukiendelea bila kuwepo kwa nyavu za kuzuia hatari (safety nets), mabomba ya maji yaliyokatika na jiko lililokuwa limebomoka, likiwa limeshakarabatiwa.

Akitoa shukrani baada ya kukabidhiwa fedha hizo, Bi. Agnes alisema anashukuru kwa kulipwa fidia hiyo ambayo ataitumia kukarabati nyumba yake. Alimshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuweka mawakili wanaotoa msaada wa kisheria ambao kwa sehemu kubwa walishiriki kutatua mgogoro huo


Mtendaji Mkuu Dkt. Maulid J. Maulid amefunga mafunzo ya uongozi na usimamizi wa shule yaliyoendeshwa kwa Wakuu wa Shule za Sekondari za Wilaya ya Arusha pamoja na viongozi wa elimu kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Arusha. 

Mafunzo hayo yameendeshwa na ADEM kwa muda wa siku tatu kuanzia tarehe 24-26 Februari, 2026 ADEM Bagamoyo.

Akifunga mafunzo hayo amewasisitiza viongozi hao wa elimu kwenda kuweka mkazo kwenye uongozi bunifu wa kimkakati unaoleta mabadiliko kama msingi wa maendeleo katika taasisi za elimu.

Pia amesisitiza juu ya uongozi jumuishi ambapo wanapaswa kushirikisha wadau, kusikiliza maoni ya jamii na kujenga mazingira ya uaminifu na uwajibikaji wa pamoja katika kufikia mafanikio ya usimamizi wa taasisi za elimu wanazozisimamia.

“Nawasihi mwende kuwa viongozi wenye maono, wenye uwezo wa kufanya maamuzi ya kimkakati, na ujuzi wa kusimamia mabadiliko ya taasisi mnazosimamia kwa ufanisi kwani ninyi ndio mtachochea mabadiliko hayo”. Ameeleza Dkt. Maulid.

Aidha, Makamu Mkuu wa Chuo Taaluma, Tafiti na Ushauri Elekezi Dkt. Lucas Mzelela amesema, mafunzo ya ADEM yamelenga kuwawezesha viongozi wa elimu kwa ujuzi wa vitendo, fikra za kimkakati na uwezo wa kusimamia taasisi za elimu kwa ufanisi ili kuleta mabadiliko ya kweli katika sekta ya elimu.

Nae Mwenyekiti wa TAHOSSA Mkoa wa Arusha, Mwalimu Omari Nyangu ameipongeza ADEM kwa namna ilivyoendesha mafunzo hayo kwa umahiri na weledi mkubwa na kutanabaisha kuwa maendeleo ya sekta ya elimu hayawezi kupatikana bila uwekezaji katika kuwajengea uwezo viongozi na wasimamizi wa taasisi za elimu na mafunzo waliyopatiwa ni dira katika usimamizi wa taasisi za elimu wanazozisimamia.

Wakuu hao wa shule wamejengewa uwezo kuhusu utawala bora wa elimu, Mpango wa Jumla wa Maendeleo ya Shule, usimamizi wa utekelezaji wa Mtaala, ustawi na usalama wa wanafunzi shuleni, ushirikishwaji wa jamii katika kuleta maendeleo ya shule, usimamizi wa rasilimali za shule, kuzingatia itifaki na huduma kwa wateja pamoja na ufuatiliaji na tathmini wa shughuli za elimu shuleni.
















RIPOTI mpya ya kimataifa imeitaja Tanzania kushika nafasi ya tano duniani kwa kuwa kizazi cha vijana ambao hawajaathiriwa na changamoto ya afya ya akili, ikizipita nchi za Ulaya, Amerika, Asia na Kusini mwa Jangwa la Sahara.

Kwa mujibu wa matokeo hayo yaliyotangazwa Washington DC kufuatia utafiti uliofanywa na taasisi ya Sapien Labs, vijana barani Afrika wameonyesha kuwa na uimara wa afya ya akili wakati dunia ikishuhudia ongezekoo kubwa la changamoto ya afya ya akili miongoni mwa vijana duniani.

Tanzania imetajwa kushika nafasi ya tano duniani huku Ghana ikishika nafasi ya kwanza kidunia, na kufuatiwa na Nigeria, Kenya, Zimbabwe, hivyo kufanya nchi zote tano za kwanza kutoka barani Afrika.

Ripoti ya Dunia ya Afya ya Akili 2025 (The Global Mind Health Report 2025) inaonesha nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara kuzipita nchi nyingi zenye kipato cha juu, huku ikionesha kuongezeka kwa tatizo la afya ya akili miongoni vijana duniani.

Utafiti huo uliotumia data zilizokusanywa kutoka watu zaidi ya milioni moja katika nchi 84 umeonyesha asilimiia 41 ya vijana walio katika umri wa utu uzima ambapo wamezama katika matumizi ya teknolojia za kidigitali, wakitegemea intaneti kwa mawasiliano, elimu, burudani na maingiliano ya kijamii (umri kati ya miaka 18-34) duniani wanakabiliwa na changamoto ya afya ya akili.

Ripoti hiyo inaonesha kuporomoka kwa uwezo wao wa ufahamu, kijamii, kushindwa kudhibiti mihemko na kupungua kwa uwezo wa kimwili ambavyo kwa kiasi kikubwa vimethiri uwezo wao wa kupambana na changamoto za maisha.

Kwa upande mwingine, ripoti hiyo inaonesha tofauti ya kikanda kwa tatizoz la afya ya akili(regional) huku baadhi ya nchi za Afrika zikiongoza kwa kupata alama za juu katika matokeo ya afya ya akili kwa vijana.

Kwa mfano, vijana waliofikia umri wa utu uzima katika eneo la Kusini mwa Jangwa la Sahara wameonesha kuwapita wenzao wanaoishi kwenye nchi zenye kipato cha juu zikiwemo za Amerika ya Kusini, Ulaya na sehemu za Asia.

Hadi kufikia mwanzoni mwa mwaka 2,000 kundi la umri wa vijana iliohusisha utafiti huo (miaka 18-34) lilifanya vizuri katika ustawi na hali nzuri ya afya ya akili likilinganishwa na makundi mengine ya umri.

“Leo hii hali imegeuka, vijana watu wazima wako katika hatari mara nne zaidi ya wale wenye umri wa zaidi ya miaka 55 kupata changamoto ya afya ya akili yenye kuhitaji matibabu, hali ambayo kwa kiasi kikubwa imeathiri uwezo wao kuzalisha katika maisha yao ya kila siku.” Inasema sehemu ya ripoti hiyo.

Ripoti ya Afya ya Akili Duniani 2025 imehusisha badiliko hilo na sababu kadhaa zikiwemo matumizi ya mapema ya simu za kiganjani wakati wa utoto, kuongezeka kwa matumizi ya vyakula na vinywaji vinavyotengenezwa viwandani kama vile soda, vyakula vilivyogansishwa na vinavyohifadhiwa kwenye vifunashio, kuporomoka kwa uhusiano wa karibu katika family na kutothamini mambo ya kiroho.

Sapien Labs ni taasisi isiyo ya faida iliyojikita katika kuelewa athari mabadiliko ya kasi ya kijamii, kiteknolojia, na mazingira ya kemikali katika ubongo na akilil ya mwanadamu. Mradi wao wa Global Mind Project ndio mkubwa zaidi unaofuatilia vipengele 47 ya afya ya akili na sababu nyingine za kimaisha na kimazingira katika nchi zaidi ya 85 kwa lugha 25.

Taasisi hiyo inaongozwa na wataalamu wa sayansi ya neva na mishipa ya fahamu, saikolojia na wale wa sayansi ya kompyuta katika kuchambua na kutatua masuala magumu ya kisayansi walikusanya data kupitia utafiti wa kimtandao uliofanywa Asia, Africa, Ulaya na Amerika.

“Hatari ya tatizo ya afya ya akili inaonekana kuwa endelevu kutoka kizazi hadi kizazi na linakwenda mbali zaidi ya kuongeza viwango vya juu vya mfadhaiko na wasiwasi,” alisema Prof Tara Thiagarajan, kiongozi wa waandaaji wa ripoti hiyo na mwanzilishi na mwanasayansi mkuu wa Sapien Labs.

“Tumetathimini uwezo wa aina mbali mbali ambao mtu anapaswa kuwa nao ili kukabili chanamoto za maisha na kugundua kuwa vijana wengi walio katika umri wa utu uzima wanahangaika. Pamoja na mifadhaiko na wasiwasi, mara nyingi wanakumbana na changagmoto za kudhibiti mihemko, kushughulikainjdwa kumudu uhusiano na wengine, na kupoteza uwezo wao wa kuelekeza akili zao katika jambo bila kuvuruga mawazo,”

Kwa mujibu wa utafiti huo, kufanya vizuri kwa baadhi ya nchi za Afrika kunaweza kumaanisha kuwa mambo ya kijamii na kifamilia yanayokuza uimara na ustawi na kupunguza athari mbayakama vile msongo wa mawazo au sababu hatarishi vinaweza kuwa vinachangia vizuri kwenye matokeo hayo.

Matokeo ya utafiti huo yanaonesha pia kuwa vijana walio katika umri wa utu uzima Kusini mwa Jangwa la Sahara wameripotiwa kuwa na uimara wa kiroho, kuchelewa kuanza matumizi ya simu za kiganjani wakati wa utoto na kuwa na uhusiano wa karibu wa kifamilia ukilinganisha na wenzao katika nchi tajiri.

Tanzania, kwa mfano, imeshika nafasi ya juu kabisa kidunia katika kipimo cha mambo ya kiroho na ndio yenye wastani wa juu wa umri wa watu waliochelewa kuanza matumizi ya simu za kiganjani licha ya kushuka kutoka nafasi ya kwanza mwaka jana hadi ya tano mwaka huu. Kenya na Nigeria pia miongoni mwa nchi ilizoshika nafasi ya juu kidunia, huku Kenya ikionesha kufanya vizuri zaidi ikilinganishwa na miaka iliyopita.

Licha ya tofauti za kikanda, tofauti ya afya ya akili kati ya wazee na vijana imeendelea duniani kote, huku wazee wakionesha kuwa na afya imara zaidi ya akili kuliko idadi ya vijana.

Utafiti uliotangulia wa Sapien Labs ulionesha kuwa tofauti hiyo ilianza kukua kabla ya mwaka 2020 na kuongezeka kwa kiasi kikubwa wakati wa janga la UVIKO-19 2020 na 2021, wakati ambao afya ya akili ya vijana wenye umri wa utu uzima (miaka kati ya 18 na 34) ilishuka kwa kasi, huku vizazi vya umri mkubwa vikiathirika kwa kiasi kidogo tu.

“Kwa miaka mitano iliyopita, tofauti hii kwa kiasi kikubwa haijabadilika,” alisema

Dr Thiagarajan, na kuongeza kuwa waandaaji wa sera wanapaswa kutazama kwa karibu athari pana za kiuchumi za kuongezeka kwa vijana wanaoingia katiika kundi la nguvukazi wakiwa na afya dhaifu ya akili,” alisema.

Huku ikigusia sababu nyinginje nyingi za kushuka kwa afya ya akili, ripoti hiyo inabainisha sababu nne za msingi zinazochangia changamoto ya afya ya akili kwa vijana duniani. Imezitaja sababu hizo kuwa ni pamoja na matumizi ya mapema ya simu wakati wa utoto, ongezeko la vyakula vya viwandani, kupunggua uhusiano wa kifamilia na kutojali mambo ya kiroho. Kila moja ya sababu hizi inahusishwa na ongezeko la hatari matatizo ya afya ya akili na kupungua kwa uwezo wa vijana kuyakabili mahitaji ya maisha.

Nchini Marekani, matumizi ya fedha kwa ajili ya utafiti wa afya ya akili na uangalizi yameongezeka sana kwa mabilioni ya dola, kama ilivyo kwa nchi za mashariki.

Na wakati hilo ni muhimu, halileti mabadiliko ya kuonekana,” alisema. “tuhahitaji kuacha kupambana na dalili na badala yake kupambana na matatizo makubwa zaidi yanayoathiri uzalishaji na ustawi wa vijana duniani. Kwa mfano, hatua za kisera zinazodhibiti upatikanaji wa simu za kiganjani kwa watoto na matumizi ya vyakula vya viwandani vinasaidia kulinda afya ya akili ya kizazi cha vijana---bila hivyo, uchumi wa dunia utatapatapa kwa miongo kadhaa ijayo.”

Ripoti hiyo pia imabainisha hatua mahususi za kisera zinazoweza kupunguza madhara, hasa madhara yanayosababishwa na matumizi ya mapema ya simu za kianjani kuongezeka kwa matumiizi ya vyakula vitokavyo viwandani. Kwa masuala yanayohusishwa na simu za kiganjani, ripoti hiyo imeshauri utungwaji wa sera zinazozuia matumizi yake wakati wa muda wa masomo na kuanzishwa kwa sharti la kuweka umri maalumu wa kutumia mitandao ya kijamii.

Kuhusu vyakuka vinanvyoandaliwa viwandani, ripoti hiyo imetaka kuwepo kwa uwekezaji mpya katiika tafiti ambazo zinaweza kufichua hatari zinahusishwa na aina mbali mbali za rangi, vikolezo, dawa za kuzuia vyakula visioze na vitu vinavyotumika kugandisha vyakula pamoja na viungio vingine vinavyopatikana kwenye vyakula na kuleta ushahidi utakaounga mkono uanzishwaji wa kanuni za kupunguza matumizi yake.

“Wakati ripoti hii si ya kwanza kuhusisha vitu hivi na changamoto za afya ya akili, upana na kina cha data ilizofanyiwa kazi na Global Minds zitasimama kuonesha ukubwaa wa matatizo vinayosababisha,” alisema Prof David Blachflower, profesa wa uchumi katika Chuo cha Dartouth. “Kwa sababu pale unapoona ushahidi kuwa karibu nusu ya vijana wote duniani---moyo wa nguvukazi---wanapambana na mlolongo wa chanamoto za afya ya akili, hii ina maana tunakabiliwa na hatari inayoweza kudhoofisha afya ya uchumi wote na jamii. Ni kiashiria cha wazi kuwa tunahitaji kuchukua hatua kushughulikia mzizi wa tatizo.”

MERIDIANBET, kampuni inazoongoza nchini katika michezo ya kubashiri na kasino mtandaoni, imeimarisha mshikamano wa kijamii kwa kutoa msaada wa vyakula na mahitaji ya msingi kwa familia zenye uhitaji maalum wilayani Kinondoni, jijini Dar es Salaam. Hatua hii ni ishara thabiti ya dhamira ya Meridianbet ya kushirikiana na jamii katika kukabiliana na changamoto za maisha ya kila siku.

Kupitia mpango wake wa Uwajibikaji kwa Jamii (CSR), Meridianbet imewekeza katika kuhakikisha ustawi wa familia unadumishwa kwa kutoa msaada wa vyakula, bidhaa za nyumbani, na mahitaji muhimu ya kila siku. Mpango huu umeundwa kwa lengo la kupunguza mzigo wa gharama zinazowakabili kaya zilizo hatarini na kutoa nafuu kwa wananchi wanaohitaji msaada wa haraka.

Meridianbet haikuachi nyuma, kuna michezo mbalimbali ya kasino mtandaoni pamoja na mechi za kimataifa za kubashiri zenye odds bomba zinazokuongezea nafasi ya kuongeza kipato chako kila siku. Kujiunga ni rahisi! Tembelea meridianbet.co.tz au piga *149*10#.

Akizungumza wakati wa zoezi la usambazaji, Nancy Ingram, msemaji wa Meridianbet, alisisitiza kuwa kampuni inaamini kuwa maendeleo ya biashara hayana maana bila maendeleo ya jamii inayozunguka. “Tunajivunia kushirikiana na wananchi na kuhakikisha msaada wetu unawafikia kwa wakati muafaka, huku tukijenga mshikamano thabiti wa kijamii,” alisema.

Wanufaika wa msaada huu walieleza furaha yao na kutoa shukrani, wakitambua kuwa msaada huo umefika wakati muafaka na kuleta faraja kubwa kwa kaya zao. Meridianbet imetangaza kuwa huu ni mwanzo wa miradi ya kijamii inayolenga afya, elimu, mazingira, na msaada kwa makundi wenye mahitaji maalum, yote kwa lengo la kujenga jamii yenye ustawi na matumaini endelevu.



Na Mwandishi Wetu, Dodoma.
TAASISI kilele ya sekta binafsi inayoshughulika na tasnia ya horticulture nchini TAHA, imewasilisha rasmi mpango wa kuandaa maonesho makubwa zaidi katika historia ya sekta ya horticulture nchini — HORTILOGISTICA AFRICA 2026 — mbele ya Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo (Mb), na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji, Kitila Mkumbo (Mb). Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Makatibu Wakuu pamoja na wajumbe wa menejimenti kutoka wizara hizo mbili.

Akiwasilisha mpango mkakati wa maandalizi ya maonesho hayo jijini Dodoma Alhamisi, Afisa Mtendaji Mkuu wa TAHA, Dkt Jacqueline Mkindi, alisema tukio hilo la kimataifa linatarajiwa kufanyika kwa mara ya kwanza nchini Tanzania mwezi Novemba 2026, likiwa na lengo la kufungua ukurasa mpya wa maendeleo ya sekta ya horticulture nchini na barani Afrika kwa ujumla.

“Mbali na manufaa mengine, maonesho haya yatafungua fursa pana za uwekezaji, kupanua masoko ya ndani na nje ya nchi, kuvutia watalii wa kibiashara, pamoja na kuimarisha ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi,” Dkt Mkindi aliwaeleza mawaziri hao.

Aliongeza kuwa HORTILOGISTICA AFRICA 2026 itakuwa jukwaa mahsusi la kuwaunganisha wadau wa sekta hiyo wakiwemo wazalishaji, wasafirishaji, watoa huduma za teknolojia, taasisi za kifedha na wanunuzi wa kimataifa, kwa lengo la kuongeza tija, ubora na ushindani wa mazao ya Tanzania katika soko la dunia.

Katika kikao hicho, Waziri wa Kilimo, Bw Chongolo, alisisitiza dhamira ya Serikali kuendelea kushirikiana kwa karibu na sekta binafsi ili kuimarisha uzalishaji, kuongeza thamani ya mazao na kuinua ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya kimataifa.

Kwa upande wake, Prof Mkumbo alisema maonesho hayo yanaendana kikamilifu na dira ya taifa ya kuvutia uwekezaji zaidi, kuzalisha ajira kwa Watanzania na kuongeza mchango wa sekta ya kilimo katika ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Kwa mujibu wa TAHA, HORTILOGISTICA AFRICA 2026 si maonesho ya kawaida ya biashara, bali ni jukwaa la kimkakati litakalounganisha wadau, teknolojia, masoko na mitaji kwa lengo la kukuza maendeleo endelevu ya sekta ya horticulture nchini.


-Mwanasheria Mkuu wa Serikali -Mgeni rasmi

-Aahidi Ushirikiano wa Kisheria katika Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira Nchini*

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeungana na wadau wa mazingira katika hafla ya futari iliyoandaliwa kwa lengo la kuimarisha ushirikiano na kuendeleza mahusiano mazuri baina ya taasisi hiyo na wadau wake.

Hafla hiyo imefanyika Leo 26, 2026 katika Hoteli ya Serena, jijini Dar es Salaam, ambapo viongozi, watumishi wa Serikali na wadau binafsi walihudhuria tukio hilo lenye taswira ya umoja na mshikamano.

Akiongea katika hafla hiyo, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Bw. Hamza S. Johari aliipongeza NEMC kwa kuandaa tukio hilo lenye kujenga umoja na kukuza mshikamano miongoni mwa Taasisi za Serikali na wadau wa mazingira. Aidha, aliahidi kuendelea kutoa ushirikiano wa kisheria ili kuhakikisha Sheria na Kanuni za mazingira zinatekelezwa ipasavyo kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware Semesi, alipozungumza alisema futari hiyo ni sehemu ya utamaduni wa Baraza katika kujenga uhusiano wa karibu na wadau wake.

Alisisitiza umuhimu wa kudumisha maadili ya utu, heshima na ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu ya hifadhi ya mazingira nchini, akibainisha kuwa kupitia ushirikiano huo malengo ya kulinda na kuboresha mazingira yanaweza kufikiwa kwa ufanisi zaidi.

Katika hatua nyingine Katibu Tawala wa Mkoa wa Dar es Salaam, Ndg. Abdul Rajabu Mhinte, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya NEMC na Ofisi ya Mkoa katika kusimamia na kutekeleza Sheria za mazingira. Aliahidi kuwa Ofisi ya Mkoa itaendelea kuunga mkono juhudi za uhifadhi na usimamizi endelevu wa mazingira kwa ustawi wa taifa.

Hafla hiyo imehudhuriwa pia na wadau wa mazingira wakiwemo JMAT, Bodi ya NEMC, watumishi wa Baraza, wawakilishi kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais pamoja na Taasisi za kibenki













Na Mwandishi Wetu

ALN Tanzania, kampuni inayojishughulisha katika huduma za kisheria na ushauri wa biashara, imezitaka biashara za kifamilia nchini kuondokana na mifumo isiyo rasmi iliyowasaidia katika hatua za awali za ukuaji, na badala yake kukumbatia mifumo thabiti ya utawala bora.

Hatua hiyo itawezesha kulinda utajiri wa vizazi, kuhakikisha ustawi wa muda mrefu na kuvutia uwekezaji kutoka nje.

Wito huo ulitolewa wakati wa hitimisho la mfululizo wa semina za mafundisho ya kusimamia biashara za kifamilia katika mfumo sahihi ( Family Business Resilience & Growth Knowledge Series), zilizoandaliwa na ALN Tanzania kwa ushirikiano na International Finance Corporation (IFC) jijini Dar es Salaam wiki hii. Mfululizo huo semina hizo tatu ulijadili misingi ya utawala wa kifamilia, muundo wa bodi na katiba za familia katika awamu zilizopita, huku kikao cha mwisho kikijikita katika urithishaji na mpito wa uongozi.

Akizungumza katika semina hiyo, Shemane Amin, Mshirika wa ALN hapa nchini , alisisitiza kuwa mwendelezo wa biashara za kifamilia hauji kwa mazoea bali unapaswa kupangwa kwa makusudi.

“Biashara nyingi za kifamilia hukua kwa mafanikio katika miaka ya mwanzo kwa kutegemea imani na maamuzi yasiyo rasmi,” alisema. “Hata hivyo, kadri biashara zinavyopanuka na vizazi vinavyoongezeka kushiriki, kuweka mifumo rasmi kunakuwa muhimu kulinda biashara yenyewe na umoja wa familia.”

Alieleza kuwa kampuni hiyo ilianzisha mfululizo huo wa semina ili kuwapatia wamiliki wa biashara za kifamilia mifumo ya vitendo kuhusu utawala bora, upangaji wa urithishaji na uwazi wa uongozi mambo ambayo mara nyingi huamua iwapo biashara itaendelea baada ya kizazi cha mwanzilishi wa biashara (Founder) katika familia husika.

Kwa upande wake, Edward Williams, Mkurugenzi wa ALN Tanzania, alisisitiza umuhimu wa kuanza mapema kupanga urithishaji na kuonya dhidi ya mabadiliko ya uongozi yanayofanyika kwa dharura.

“Moja ya dhana potofu iliyoenea katika biashara za kifamilia ni kwamba urithishaji huanza pale mwanzilishi anapokuwa tayari kustaafu,” alisema. “Kwa uhalisia, urithishaji huanza mapema zaidi.

Mabadiliko yenye mafanikio ni yale ambayo ukuzaji wa uongozi, miundo ya wanahisa na mifumo ya utawala inakuwa tayari imewekwa tangu awali.”, alisema.

Alibainisha kuwa kadri biashara za Kitanzania zinavyokua kwa thamani na kuwa tata zaidi, mikataba rasmi ya wanahisa, katiba za familia, majukumu yaliyoainishwa wazi kwa watendaji wakuu na mifumo huru ya usimamizi vinakuwa muhimu katika kulinda thamani ya muda mrefu.

Naye Mona Doshi, Mshirika wa ALN kutoka Mombasa nchini Kenya, alizungumzia umuhimu wa sera rasmi za ajira kwa wanafamilia katika kuimarisha uimara wa biashara.

“Kadri familia zinavyopanuka kizazi hadi kizazi, kuwa na mwongozo wa uwazi kuhusu vigezo vya kuajiriwa, viwango vya utendaji na uwajibikaji husaidia kuzuia migogoro ya ndani na kuimarisha uongozi unaozingatia sifa,” alieleza.

Aliwahimiza wamiliki wa biashara kuweka mifumo rasmi ya utawala inayolinda urithi wa familia huku ikizingatia weledi, ili kuhakikisha mabadiliko ya uongozi yanategemea maandalizi na uwezo wa mtu badala ya kuchaguliwa kuongoza tu kwa sababu ni sehemu ya familia.

Akizungumza kwa niaba ya IFC, Rose Lumumba alisisitiza kuwa utawala bora uliowekwa kwa mifumo rasmi unahusishwa moja kwa moja na utayari wa kupokea uwekezaji na ustawi wa muda mrefu.

“Biashara za kifamilia zinazoweka mifumo ya utawala mapema huwa katika nafasi nzuri zaidi ya kuvutia mitaji, kupanuka kwa uwajibikaji na kustahimili mabadiliko ya vizazi,” alisema.

Washiriki walikubaliana kuwa biashara za kifamilia zina mchango mkubwa katika uchumi wa Tanzania, na kwamba uwezo wake wa kuweka mifumo rasmi ya uongozi na utawala utaathiri uimara wa sekta binafsi kwa ujumla.

Tafiti za kimataifa zinaonesha kuwa ingawa biashara za kifamilia zinachangia zaidi ya asilimia 60 ya shughuli za sekta binafsi duniani, ni takriban asilimia 30 tu zinazofanikiwa kuvuka hadi kizazi cha pili, na chini ya asilimia 15 hufikia kizazi cha tatu. Wataalamu wa sekta hiyo wanaeleza kuwa upangaji madhubuti wa urithishaji na nidhamu ya utawala bora huongeza kwa kiasi kikubwa uwezekano wa mafanikio ya mpito huo.

ALN Tanzania hutoa ushauri kwa biashara za kifamilia kuhusu uundaji wa mifumo ya utawala, mipango ya urithishaji, makubaliano ya wanahisa na suluhisho za usimamizi wa utajiri wa kuvuka mipaka, ikiwawezesha kubadilika kutoka biashara zinazoongozwa na waanzilishi hadi taasisi imara za kudumu.
Bi. Shemane Amin, Mshirika wa ALN Tanzania (kulia), akiendesha mazungumzo na Bw. Vineet Verma, Meneja Mkuu wa Kioo Limited, wakati wa hitimisho la mfululizo wa Uendeshaji kimfumo wa biashara za kifamilia ( Family Business Resilience & Growth Knowledge Series), ulioandaliwa kwa ushirikiano kati ya ALN na International Finance Corporation (IFC) jijini Dar es Salaam wiki hii.
Bw. Edward Williams, Mkurugenzi wa ALN Tanzania, akiongea wakati wa hitimisho la mfululizo wa kongamano la mafunzo ya uendeshaji kimfumo wa biashara za kifamilia (Family Business Resilience & Growth Knowledge Series), ulioandaliwa kwa ushirikiano kati ya ALN na International Finance Corporation (IFC) jijini Dar es Salaam wiki hii.

Baadhi ya washiriki wa hitimisho la mfululizo wa kongamano la mafunzo ya uendeshaji bora wa biashara za kifamilia ( Family Business Resilience & Growth Knowledge Series), ulioandaliwa na ALN Tanzania kwa ushirikiano na International Finance Corporation (IFC) jijini Dar es Salaam wiki hii.

📍Yataja utendaji wake kama kiungo muhimu kwenye chama na serikali

*NA MWANDISHI WETU, MBEYA

Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Mbeya Vijijini, imemtunukia Tuzo maalum ya Heshima na Shukrani Mkuu wa Wilaya hiyo, Mhe. Solomon Itunda, kwa kutambua mchango wake mkubwa wa kuunganisha Serikali na Chama katika utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2020-2025.

Tuzo hiyo imekabidhiwa jana tarehe 26 Februari 2026, wakati wa kikao cha Halmashauri Kuu ya Wilaya kilichopokea na kujadili taarifa ya utekelezaji wa Ilani kwa kipindi cha mwezi Julai hadi Desemba 2025.

Akisoma maelekezo ya Kamati ya Siasa mbele ya wajumbe wa Halmashauri Kuu, Mwenyekiti wa CCM Wilaya Hakimu Mwalupimbi, amemuelezea DC Itunda kama "Kiungo" madhubuti ambaye amekuwa akipatikana wakati wote kushughulikia kero za wananchi na mahitaji ya Chama bila kujali muda.

"DC Itunda umekuwa kiungo kikubwa baina ya Chama na Serikali. Iwe usiku wa manene, asubuhi au mchana, umekuwa ukipokea simu na pale unapokuwa na majukumu mengine unajibu kwa ujumbe mfupi na baadaye unapiga simu kufuatilia. Hiyo ni ishara ya kiongozi aliyelelewa na kukomaa ndani ya Chama," alisema Mwenyekiti huyo.

Mwenyekiti aliongeza kuwa uzoefu wa DC Itunda uliotukuka—kuanzia nafasi ya Katibu wa CCM Mkoa wa Mbeya hadi ngazi ya Taifa—umechangia kwa kiasi kikubwa utulivu na mafanikio yanayoonekana sasa wilayani humo.

 Alisisitiza kuwa tuzo hiyo ni ishara ya upendo na shukrani kutoka kwa wana-CCM ili kumtia moyo aendelee kukibeba Chama, hususan katika nyakati hizi za kuelekea majukumu mazito ya kitaifa.

Akizungumza kwa unyenyekevu baada ya kupokea tuzo hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Mhe. Solomon Itunda, amekishukuru Chama Cha Mapinduzi kwa malezi yaliyomfikisha katika nafasi hiyo ya utumishi wa umma.

Kamati ya Siasa ya Wilaya imebainisha kuwa utaratibu huo wa kutambua na kupongeza watendaji wanaofanya vizuri utakuwa endelevu ili kuongeza ari ya utumishi ndani ya Wilaya ya Mbeya.







 


Top News