Na Farida Mangube 

Mbunge wa Jimbo la Ulanga, Salim Alaudin Hashim, ameiomba Serikali kuharakisha ujenzi wa kipande cha barabara ya Lupiro–Mahenge, akisema ni muhimu kwa usafirishaji wa mazao ya kilimo na madini katika Wilaya za Ulanga na Malinyi, Mkoa wa Morogoro.

Ametoa ombi hilo wakati wa hafla ya kumkabidhi mkandarasi kazi ya ujenzi wa Daraja la Namuhanga lililopo Tarafa ya Lupiro. Daraja hilo lilisombwa na mafuriko, jambo lililosababisha usumbufu mkubwa kwa wananchi wa Wilaya za Ulanga na Malinyi.

Mbunge Salim amesema ana imani ujenzi wa daraja hilo utakamilika kwa wakati kabla ya kuanza kwa msimu ujao wa mvua, ili kurahisisha shughuli za kiuchumi, hasa kilimo ambacho ndicho tegemeo kuu la wananchi wa maeneo hayo.

«“Tunashukuru sana Serikali kwa kutuona sisi wananchi wa Wilaya za Ulanga na Malinyi. Wananchi sasa wanaenda kuondokana na adha iliyokuwa ikiwapata kutokana na kusombwa kwa Daraja la Namuhanga,” amesema Mbunge Salim.»

Kwa upande wake, Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, amesema Mkoa wa Morogoro ni miongoni mwa maeneo yenye changamoto kubwa za miundombinu ya barabara na madaraja, lakini Serikali imejipanga kuhakikisha changamoto hizo zinapatiwa ufumbuzi.

Akizungumzia mradi wa barabara ya Lupiro–Malinyi, Waziri Ulega amesema tayari fedha za ujenzi kwa kiwango cha lami zimetengwa na mkandarasi anatarajiwa kuanza kulipwa malipo ya awali wakati wowote ili kazi ianze rasmi.

"Nyinyi wakazi wa Wilaya hizi mbili ni wazalishaji wakuu wa chakula hapa nchini. Serikali imedhamiria kuhakikisha tunamaliza tatizo hili la miundombinu, hasa barabara ambazo zitajengwa kwa kiwango cha lami ili kuwaondolea changamoto za usafiri na usafirishaji,” amesema Waziri Ulega."

Ujenzi wa barabara na madaraja katika eneo hilo unatarajiwa kuongeza urahisi wa usafirishaji wa mazao, kuchochea biashara na kuimarisha maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi wa Ulanga na Malinyi.



Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Mhe. Mussa Kilakala, ameipongeza Wizara ya Nishati kwa kuandaa Warsha ya Nishati Safi ya Kupikia kwa wanahabari na Maafisa habari, akisema mafunzo hayo ni hatua muhimu ya kuhakikisha elimu sahihi inawafikia wananchi na kuimarisha utekelezaji wa ajenda ya matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.

Akizungumza Julai 14, 2026 wakati wa ufunguzi wa Warsha ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari, Maafisa Mawasiliano Serikalini wa Mikoa, Taasisi, Wizara pamoja na Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Nishati kuhusu uandishi na uhamasishaji wa masuala ya nishati safi ya kupikia inayofanyika katika Ukumbi wa Morena Hotel mkoani Morogoro amesema Mkoa wa Morogoro una vyanzo vingi vya maji vinavyopaswa kulindwa, hivyo ajenda ya kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia itasaidia kuhifadhi mazingira kwa kupunguza ukataji wa miti, kulinda afya za wananchi pamoja na kutunza vyanzo hivyo vya maji kwa manufaa ya kizazinkijacho.

Amesema elimu inayotolewa kupitia warsha hii ikiwafikia wananchi kwa usahihi, itasaidia kuongeza uelewa kuhusu maana na faida za nishati safi ya kupikia, hususan kwa jamii za vijijini, jambo litakalowezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika juhudi za kulinda mazingira na kutumia nishati salama na nafuu.

Mhe. Kilakala amewataka washiriki kutoka Mikoa mbalimbali nchini kutumia maarifa waliyoyapata katika warsha hiyo kwa weledi mkubwa wanaporejea kwenye maeneo yao ya kazi kwani mafunzo haya yataongeza hamasa na kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanafikiwa na elimu ya nishati safi ya kupikia na hivyo kuchangia kufikiwa kwa malengo ya taifa ya kuhakikisha asilimia 80 ya wananchi wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo 2034.










-Teknolojia, usuluhishi wa migogoro na maboresho ya sheria vipaumbele vya mafunzo

-Mawakili wakumbushwa kulinda maslahi ya Taifa, uwekezaji na usalama wa nchi

 -Mafunzo yatekeleza maelekezo ya Rais Samia ya kupitia na kuboresha sheria


Na Vero Ignatus, Michuzi TV – Arusha

Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza S. Johari, leo Julai 14, 2026 amefungua rasmi mafunzo ya siku tatu kwa mawakili 650 wa Serikali yanayofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC). Mafunzo hayo yanalenga kuwaimarisha mawakili katika utekelezaji wa majukumu yao sambamba na maandalizi ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Akizungumza wakati wa ufunguzi, Mhe. Johari alisema mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo mawakili kuhusu mabadiliko yanayotokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia, pamoja na kuhakikisha mfumo wa sheria unaendana na malengo ya Dira ya Maendeleo 2050 ili uwe kichocheo cha maendeleo ya Taifa.

Alisema mada zitakazojadiliwa zinahusisha usuluhishi wa migogoro, hususan migogoro ya kibiashara, namna ya kuweka uwiano kati ya maendeleo ya nchi na ulinzi wa wawekezaji, pamoja na kutathmini kama sheria zilizopo zinachochea mageuzi ya uchumi na maendeleo endelevu.

"Tunataka pia kuangalia jukumu la wakili katika kuimarisha uzalendo, kulinda maslahi pamoja na usalama wa Taifa. Wasipofahamu wajibu huo wanaweza kujikuta wanaingia katika matendo yanayoweza kuhatarisha usalama wa Taifa au kuathiri maslahi ya nchi kiuchumi na kijamii," alisema Mhe. Johari.

Awali, Mkurugenzi wa Uratibu na Huduma za Ushauri wa Sheria, Wakili Neema Ringo, alisema mafunzo hayo yatawawezesha mawakili kuongeza uelewa kuhusu matumizi ya teknolojia, kutambua vihatarishi vinavyotokana na maendeleo ya kidijitali, pamoja na kujadili namna ya kuboresha sheria ili ziendane na mazingira ya sasa.

Alieleza kuwa mafunzo hayo pia yanatekeleza maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, aliyemtaka Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuratibu mapitio ya sheria zote ili kufanyiwa marekebisho, kuboreshwa au kufutwa pale zinaposhindwa kuendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Wakili Ringo aliongeza kuwa mafunzo hayo, yaliyoandaliwa na kuratibiwa na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, yanatoa fursa kwa mawakili kubadilishana uzoefu, kuongeza ujuzi na kujadili mabadiliko ya sheria, sayansi na teknolojia yanayoendelea duniani.

Kwa upande wake, Mwandishi Mkuu wa Sheria, Onorious Njole, alisema jumla ya mawakili 650 kutoka wizara, taasisi za Serikali, mamlaka za Serikali za Mitaa na idara mbalimbali za umma wanashiriki mafunzo hayo. Alisema lengo ni kuwajengea uwezo wa kitaaluma na kiutendaji ili waendelee kusimamia kwa ufanisi tasnia ya sheria na kuchangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.







Skauti Mkuu wa Tanzania, Lt. Rashid Mchata, amesema ushirikiano kati ya Chama cha Skauti Tanzania (Tanzania Scouts Association-TSA) na Oryx Gas Tanzania Limited ni hatua ya kimkakati itakayowawezesha maelfu ya vijana wa Skauti na Watanzania kwa ujumla kupata maarifa, ujuzi na fursa za kushiriki katika maendeleo ya Taifa kupitia matumizi salama ya nishati safi.

Akizungumza katika hafla ya utiaji saini wa mkataba wa ushirikiano huo leo Jumatano Julai 15, 2026, Lt. Mchata amesema hafla hiyo si tukio la kawaida la kusaini hati, bali ni tamko la dhamira, daraja la fursa na mwanzo wa safari ya pamoja ya kuwaletea vijana mabadiliko chanya yatakayodumu kwa miaka mingi.

Amesema TSA inaamini kuwa kijana mwenye maarifa ni nguvu ya Taifa, mwenye ujuzi ni rasilimali muhimu ya maendeleo, huku mwenye maadili na nidhamu akiwa msingi wa mustakabali wa Tanzania.

Lt. Mchata ameeleza kuwa kupitia makubaliano hayo, Skauti Tanzania itaunganisha mtandao wake mkubwa wa vijana na utaalamu wa Oryx Gas Tanzania katika sekta ya gesi ya LPG ili kuimarisha elimu ya matumizi salama ya nishati safi, usalama wa jamii, maandalizi ya kukabiliana na dharura pamoja na kuwaongezea vijana ujuzi utakaowawezesha kujiajiri na kupata ajira.

Amesisitiza kuwa, lengo si kuwaeleza vijana kuhusu fursa zilizopo pekee, bali kuwajengea uwezo wa kuzitambua, kuzitumia na kuzalisha fursa mpya zinazochochea maendeleo ya Taifa.

Aidha, amesema TSA itasimamia utekelezaji wa ushirikiano huo kwa uwajibikaji mkubwa ili kuhakikisha unaleta matokeo yaliyokusudiwa, huku akiwataka vijana wa Skauti kutumia nafasi hiyo kujifunza, kujenga uwezo na kuwa wabunifu katika kulitumikia Taifa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Oryx Energies Tanzania, Benoit Araman, amesema kampuni hiyo imeamua kushirikiana na Skauti baada ya kuona kuwa harakati zao zina misingi inayolingana na malengo ya Oryx ya kuitumikia jamii kupitia elimu ya matumizi salama ya gesi ya LPG.

Amesema dhima ya Skauti ya kuwa tayari wakati wote kuhudumia jamii ndiyo iliyowafanya kuitambua TSA kama mshirika sahihi wa kutekeleza programu ya utoaji elimu kuhusu matumizi salama ya gesi kwa wananchi.

Araman ameongeza kwa kusema kuwa, Oryx kwa kushirikiana na wataalamu wake itatoa mafunzo kwa wawakilishi wa Skauti kutoka maeneo mbalimbali nchini, ambao baadaye watakuwa wakufunzi na mabalozi wa kuielimisha jamii namna sahihi ya kutumia gesi ya LPG kwa usalama.

Amesema hatua hiyo itasaidia kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu matumizi salama ya nishati safi, kupunguza ajali zinazotokana na matumizi yasiyo sahihi ya gesi na kuchangia ustawi wa jamii kwa muda mrefu.

Naye Kamishna Mkuu wa Skauti Tanzania, Abubakari Mtitu, amesema, mkataba huo ni sehemu ya mkakati endelevu wa kuhakikisha vijana wanapata mafunzo ya weledi kuhusu matumizi ya nishati safi na tahadhari zinazopaswa kuzingatiwa wakati wa matumizi yake.

Ameendelea kwa kusema kuwa, ushirikiano huo unaendana na misingi ya Skauti ya kutekeleza wajibu kwa Mungu, kwa wengine na kwa nafsi binafsi, huku ukiwapa vijana nafasi ya kutumia elimu watakayopata kuwahudumia wananchi katika maeneo yao.

Mtitu amesema kupitia mafunzo hayo, vijana wa Skauti pamoja na vijana wengine wa Tanzania watawezeshwa kuwa mabalozi wa matumizi salama ya nishati safi, hatua itakayochangia kujenga jamii salama na kuifanya dunia kuwa mahali bora zaidi kuliko walivyoikuta.

Ameongeza kwa kusema kuwa, TSA itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuandaa programu zinazowajengea vijana uwezo, maadili na ujuzi unaohitajika katika kuchangia maendeleo endelevu ya Taifa.










Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini yanatarajiwa kuongezeka kwa kasi endapo wananchi wataendelea kupata taarifa sahihi, zinazoeleweka na zinazotolewa kwa ujumbe mmoja kutoka kwa wadau mbalimbali wanaohusika na sekta hiyo.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Nishati Safi ya Kupikia,  Nolasco Mlay, wakati wa ufunguzi wa Warsha ya Kuwajengea Uwezo Waandishi wa Habari na Maafisa Mawasiliano wa Serikali kutoka mikoa, wizara, taasisi na mashirika yaliyo chini ya Wizara ya Nishati kuhusu uandishi na uhamasishaji wa matumizi ya nishati safi ya kupikia. Warsha hiyo imefanyika Julai 14, 2026 mkoani Morogoro.

 Mlay amesema utoaji wa ujumbe sahihi na wenye uelewa wa pamoja ni nyenzo muhimu katika kuwasaidia wananchi kufanya maamuzi sahihi kuhusu matumizi ya teknolojia mbalimbali za nishati safi ya kupikia, ikiwemo gesi ya kupikia (LPG), umeme, biogesi, gesi asilia na mkaa mbadala.

Amesema Serikali inaendelea kutekeleza Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia wenye lengo la kuhakikisha kuwa ifikapo mwaka 2034, angalau asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia.

Kwa mujibu wa Mlay, baada ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kuzindua Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia mwaka 2024, Serikali iliendelea kuimarisha juhudi hizo kwa kuzindua Mkakati wa Mawasiliano mwaka 2025, unaolenga kuhakikisha ujumbe unaotolewa kwa wananchi kuhusu nishati safi ya kupikia unakuwa wa pamoja, sahihi na unaoeleweka.

Ameeleza kuwa mkakati huo unalenga kuwawezesha wadau wote wanaotoa elimu kwa umma kuwa na uelewa unaofanana ili kuondoa taarifa zinazokinzana, kuongeza uhamasishaji na kuwafanya wananchi kuchagua matumizi ya nishati safi kwa manufaa ya afya zao, mazingira na maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

 Mlay amesisitiza kuwa vyombo vya habari vina nafasi ya kipekee katika kufanikisha ajenda hiyo ya kitaifa, kwani vina uwezo mkubwa wa kufikisha ujumbe kwa mamilioni ya Watanzania na kuongeza uelewa kuhusu faida za matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Aidha, amewataka waandishi wa habari pamoja na Maafisa Mawasiliano wa Serikali kuendelea kuandika na kusambaza taarifa zenye usahihi, zinazozingatia ujumbe wa pamoja na zinazohamasisha mabadiliko ya tabia, akibainisha kuwa hatua hiyo itasaidia kupunguza upotoshaji, kuongeza uelewa wa jamii na kuharakisha utekelezaji wa malengo ya taifa ya matumizi ya nishati safi ya kupikia.



Na MWANDISHI WETU

UONGOZI mpya wa Taasisi ya Usanifu wa Kiswahili na Ushairi Tanzania (UKUTA) leo umekabidhiwa rasmi ofisi na uongozi uliopita baada ya uchaguzi mkuu uliofanyika Julai 11 mwaka huu.

Akizungumza katika hafla ya makabidhiano hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa Anatouglou, jijini Dar es Salaam, yalipo makao makuu ya UKUTA, Mwenyekiti wa taasisi hiyo taifa, Hussein Ally Jimbika, amesema , wamejipanga kusimamia kikamilifu usanifu wa lugha ya Kiswahili na ushairi nchini.

Amesema, UKUTA itaendelea kuenzi jitihada za kubwa za viongozi na waasisi wa taasisi hiyo hususan Baba wa Taifa hayati Mwalimu Julius Nyerere, ambaye ndiyo mtu wa kwanza kuunda chombo hiki kabla ya uhuru kwa kushirikiana na hayati Abeid Aman Karume na Sheikh Amri Abeid Karuta.

Ameeleza UKUTA ilitoa mchango mkubwa katika kufanikisha taifa kupata uhuru na kwamba uongozi wa taasisi hiyo utaendelea kufuata nyendo zao kuhakikisha safari ya kuenzi Kiswahili inafanikiwa.

“Wazee hawa walikuwa na makusudio makubwa ya Kiswahili kuwa ni nyenzo muhimu ya kupata uhuru na ustawi wa taifa.

Hivyo Uongozi mpya tutashirikiana na wenzetu kuhakikisha lengo la waasisi hawa linaendelewa na kufikiwa katika kukuza Kiswahili,”amesema Jimbika.

Jimbika alisema lengo lingine ni kuongeza usajili wa wanachama kwani mpaka sasa UKUTA inawachama 2050 tu.

Katibu Mkuu wa UKUTA, Abubakyr Kiaibamba, amewarika wanachama wa katika ofisi za makao makuu ya taasisi hiyo zilizopo katika jengo la Anatouglou kwa uratibu wa shughuli zote za taasisi na kujisajili .

“Malengo yangu ni kuhakikisha tunakifanya Kiswahili kuwa bidhaa. Hii ndiyo kazi anayoifanya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan. Tutahakikisha vitabu vinaandikwa, mashairi yanatungwa na tunawakomboa washairi kuchumi kupitia kazi zao,”amesema Kiaibamba.

Akikabidhi nyaraka za ofisi Katibu Mkuu mstaafu Hassan Ligile, ameupongeza uongozi huo mpya kushinda katika uchaguzi wa kidermokrasia uliofanyika na kwamba wataendelea kutoa ushirikiano kuhakikisha UKUTA inasonga mbele huku akijivunia mafanikio yaliyopatikana chini ya uongozi wake.









Jane Mwakyoma, July 15, 2026, Rukwa.

MKUU wa Mkoa wa Rukwa Charles Makongoro Nyerere ameipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi kwa kufanikiwa kupata hati safi akieleza kuwa mafanikio hayo ni kielelezo cha usimamizi bora wa fedha za umma na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu ya Serikali.

Nyerere ametoa pongezi wakati akizungumza katika Baraza Maalum la Madiwani la kujadili Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).

Amesema mafanikio hayo yametokana na ufungaji mzuri wa vitabu vya hesabu za Serikali, uzingatiaji wa sheria, kanuni na taratibu za matumizi ya fedha za umma, usimamizi madhubuti wa rasilimali, ukusanyaji mzuri wa mapato, utekelezaji wa bajeti kwa ufanisi, pamoja na ushirikiano imara kati ya Menejimenti ya Halmashauri na wadau mbalimbali wa maendeleo.

Aidha amesisitiza kuwa mafanikio hayo yanaendelea kuimarisha uwajibikaji, uwazi na usimamizi bora wa rasilimali za umma kwa manufaa ya wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi.

Pia ameitaka Halmashauri kuendeleza juhudi hizo ili kudumisha viwango vya utendaji na utoaji bora wa huduma kwa wananchi.








Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali inaendelea kutekeleza miradi mikubwa ya maji ili kumaliza tatizo la upatikanaji wa maji safi na salama katika mikoa yote ya Zanzibar.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 15 Julai 2026, Ikulu Zanzibar, alipokutana na Waziri wa Maji, Nishati na Madini Zanzibar, Mhe. Nadir Abdullatif, pamoja na Waziri wa Maji wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jumaa Aweso.

Amesema miradi ya maji tayari imeanza kuleta matokeo katika mikoa ya Kaskazini Unguja, Kusini Unguja na Mjini Magharibi, huku akisisitiza matumizi ya teknolojia za kisasa na kuimarisha ushirikiano kati ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za maji.

Kwa upande wake, Waziri wa Maji wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jumaa Aweso, ameahidi kuendelea kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika utekelezaji wa miradi ya maji na kueleza kuwa wizara yake imeandaa mfumo wa kidijitali utakaowezesha wananchi kutoa taarifa za changamoto za huduma ya maji ili zipatiwe ufumbuzi kwa haraka.

Vilevile, amempongeza Rais Dkt. Mwinyi kwa utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo inayosimamiwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.










Na Oscar Assenga,MKINGA

JUMUIYA ya Afrika Mashariki (EAC) imeeleza itaendelea kuimarisha utekelezaji wa Mfumo Rahisi wa Biashara (Simplified Trade Regime-STR) ili kurahisisha biashara za mipakani, kuwawezesha wafanyabiashara wadogo kuongeza uzalishaji, kupanua masoko ya bidhaa zinazozalishwa ndani ya ukanda na kupunguza gharama za biashara.


Kauli hiyo ilitolewa na Naibu Katibu Mkuu wa EAC anayeshughulikia Forodha, Biashara na Fedha, Annette Semuwamba, wakati alipotembelea Kituo cha Huduma cha Pamoja Mpakani (One Stop Border Post-OSBP) cha Horohoro wilayani Mkinga, mkoani Tanga.


Ziara hiyo ni sehemu ya tathmini ya utekelezaji wa Mfumo Rahisi wa Biashara katika vituo saba vya Huduma vya Pamoja Mpakani vilivyopo ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Semuwamba alisema EAC itaendelea kushirikiana na nchi wanachama na wadau mbalimbali kuhakikisha wafanyabiashara wadogo wanaovuka mipaka wanapata mazingira rafiki kupitia taratibu rahisi za forodha.

“Tumefurahishwa kuona biashara kati ya nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki inaendelea kukua. Kinachotutia moyo zaidi ni kwamba bidhaa nyingi zinazovuka mipaka ni bidhaa zinazozalishwa ndani ya ukanda wetu,” alisema.

Alisema uwekezaji uliofanywa katika miundombinu ya vituo vya Huduma vya Pamoja Mipakani umechangia kupunguza muda wa kuhudumia mizigo na wasafiri, kupunguza gharama za biashara na kusaidia kushusha bei za bidhaa kwa walaji.

Aidha, aliipongeza Serikali ya Tanzania kwa kufunga mashine ya kisasa ya ukaguzi wa mizigo (scanner) katika mpaka wa Horohoro/Lunga Lunga, akisema hatua hiyo itaharakisha ukaguzi na uondoshaji wa mizigo.

Semuwamba alipendekeza pia kuanzishwa kwa mfumo wa kubadilishana picha za mizigo iliyokaguliwa kwa kutumia mashine hizo kati ya vituo vya Huduma vya Pamoja Mipakani ili kupunguza gharama za uwekezaji wa vifaa hivyo katika maeneo mengine ya mipakani.

Awali, Mkuu wa Kituo cha Huduma cha Pamoja Mpakani Horohoro, Shadrack Mbonea, alisema kituo hicho kimechangia kwa kiasi kikubwa kurahisisha biashara na usafirishaji wa mizigo kati ya Tanzania na Kenya.

Alisema Horohoro ni miongoni mwa vituo saba vya Huduma vya Pamoja Mipakani nchini vinavyowezesha wasafiri, magari na mizigo kupata huduma zote za mipakani katika eneo moja badala ya kuhudumiwa kila upande wa mpaka.

“Kituo hiki kilianza majaribio ya utoaji wa huduma kwa mfumo wa One Stop Border Post mwezi Septemba 2021 na tangu wakati huo kimeendelea kufanya kazi kwa mafanikio makubwa,” alisema.

Mbonea alisema kituo hicho kina taasisi 19 za Serikali zinazoongozwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), zikiwemo Idara ya Uhamiaji, Jeshi la Polisi, Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA), Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA), TASAC, Tume ya Madini, Idara ya Uvuvi, Idara ya Mifugo, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).

Alisema taasisi hizo zina jukumu la kukusanya mapato ya Serikali, kurahisisha biashara, kulinda jamii dhidi ya bidhaa hatarishi, kutekeleza sera za biashara, kukusanya takwimu za biashara za mipakani na kudhibiti magendo.

Kwa mujibu wa Mbonea, hapo awali mfumo wa OSBP ulikuwa ukifanya kazi kwa saa 12 kwa siku, hali iliyowalazimu wasafiri na wasafirishaji wa mizigo kukamilisha taratibu za forodha katika kila upande wa mpaka.

Alisema kupitia makubaliano kati ya Tanzania na Kenya, huduma sasa zinatolewa kwa saa 24, hatua iliyopunguza muda wa kusubiri na kuongeza ufanisi wa utoaji huduma.

Aidha, alisema kituo hicho kinatekeleza Mfumo Rahisi wa Biashara unaowawezesha wafanyabiashara wadogo wanaosafirisha bidhaa zenye thamani isiyozidi dola za Marekani 2,000 kutumia taratibu rahisi za forodha.

“Tumeanzisha dawati maalumu la kuwahudumia wafanyabiashara wadogo, tumerahisisha utaratibu wa ukadiriaji wa kodi kwa kutumia fomu ya F88 na tunatambua Vyeti Rahisi vya Asili ya Bidhaa vinavyotolewa na mamlaka za Kenya,” alisema.

Aliongeza kuwa kituo hicho pia kinatekeleza Mfumo wa Himaya Moja ya Forodha wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (Single Customs Territory-SCT), ambao umechangia kupunguza muda wa uondoshaji wa mizigo, kushusha gharama za biashara na kuondoa vikwazo vya biashara ndani ya ukanda.

Alisema ushirikiano kati ya Horohoro na Lunga Lunga umeimarisha mapambano dhidi ya magendo kupitia doria za pamoja, mikutano ya kila robo mwaka na utoaji wa elimu kwa wafanyabiashara kuhusu taratibu za biashara za mipakani.

Takwimu zinaonyesha kuwa thamani ya bidhaa zinazouzwa nje kupitia mpaka wa Horohoro/Lunga Lunga imeongezeka kutoka Sh milioni 306.4 mwaka wa fedha 2022/23 hadi Sh milioni 548 mwaka 2024/25. Aidha, thamani ya bidhaa zinazoingizwa nchini kupitia mpaka huo imeongezeka kutoka Sh milioni 134.7 hadi Sh milioni 175.9 katika kipindi hicho.

Ongezeko hilo linaakisi mafanikio ya juhudi za EAC na nchi wanachama katika kuimarisha biashara za mipakani, kuongeza ushindani wa bidhaa zinazozalishwa ndani ya ukanda na kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi kati ya Tanzania na Kenya.

Top News