Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (kushoto), akisalimiana na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya TCB, Bw. Adam Mihayo, mara baada ya Bw. Laiser pamoja na ujumbe wake kumtembelea ofisini kwake, jijini Dar es Salaam jana, kwa mazungumzo yenye lengo la kuimarisha mahusiano ya ushirikiano wa kimkakati kati ya taasisi hizo mbili katika kuangalia fursa za kibiashara.

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (kushoto), akimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya TCB, Bw. Adam Mihayo, mara baada ya Bw. Laiser pamoja na ujumbe wake kumtembelea ofisini kwake jijini Dar es Salaam jana, kwa mazungumzo yenye lengo la kuimarisha mahusiano ya ushirikiano wa kimkakati kati ya taasisi hizo mbili katika kuangalia fursa za kibiashara.

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (wa pili kushoto), akizungumza na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya TCB, Bw. Adam Mihayo (kushoto), pamoja na baadhi ya maofisa wa benki hiyo, mara baada ya Bw. Laiser pamoja na ujumbe wake kumtembelea ofisini kwake jijini Dar es Salaam jana, kwa mazungumzo yenye lengo la kuimarisha mahusiano ya ushirikiano wa kimkakati kati ya taasisi hizo mbili katika kuangalia fursa za kibiashara.





Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (wa nne kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya TCB, Bw. Adam Mihayo (wa tano kushoto), pamoja na baadhi ya maofisa kutoka benki zote mbili, wakipiga picha ya kumbukumbu mara baada ya Bw. Laiser pamoja na ujumbe wake kutembelea ofisini za TCB, jijini Dar es Salaam jana, kwa mazungumzo yenye lengo la kuimarisha mahusiano ya ushirikiano wa kimkakati kati ya taasisi hizo mbili katika kuangalia fursa za kibiashara.


Na. Peter Haule, WF, Arusha

Serikali imesema matumizi ya Mfumo wa Kielektroniki wa Ununuzi wa Umma (NeST) yameendelea kuongezeka nchini, hatua iliyochangia kuimarika kwa uwazi, ushindani, uwajibikaji na matumizi yenye tija ya fedha za umma katika shughuli za ununuzi na ugavi.

Hayo yalielezwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), katika hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila, wakati wa Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma 2026 lililofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).

Alisema kuwa hadi Juni 30, 2026, jumla ya wazabuni 45,270 walikuwa wameidhinishwa na kusajiliwa katika Mfumo huo, ambapo asilimia 95 kati yao walikuwa wazabuni wa ndani.

“Katika mwaka wa fedha 2025/2026, hadi Juni 30, 2026, jumla ya tuzo za zabuni 181,057 zenye thamani ya shilingi trilioni 14.5 zilitolewa kupitia mfumo wa NeST, hatua inayoonesha kuongezeka kwa matumizi ya Mfumo huo katika utekelezaji wa shughuli za ununuzi wa umma”, alisema Dkt. Nguvila.

Dkt. Nguvila alisema mafanikio hayo yanaonesha kuwa NeST imeendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuimarisha usimamizi wa shughuli za ununuzi wa umma na ugavi, pamoja na kuongeza uwazi, ushindani na thamani ya fedha za umma.

Alisema Mfumo huo pia umeipa Tanzania heshima kimataifa baada ya kuchaguliwa kuwa miongoni mwa Mifumo 20 bora ya Serikali duniani katika Tuzo za World Summit on the Information Society, mafanikio yanayoakisi hatua kubwa iliyopigwa katika mageuzi ya kidijitali kwenye sekta ya ununuzi wa umma na ununuzi endelevu.

Dkt. Nguvila alifafanua kuwa, ujenzi wa Mfumo wa NeST umekamilika kwa asilimia 100 na kwa sasa shughuli zote muhimu za ununuzi wa umma, kuanzia usajili wa wazabuni, uandaaji wa zabuni, usimamizi wa mikataba hadi malipo, zinafanyika kupitia Mfumo huo.

Alisisitiza kuwa taasisi zote za umma zina wajibu wa kutekeleza shughuli za ununuzi kupitia Mfumo wa NeST, akionya kuwa taasisi yoyote itakayofanya ununuzi nje ya Mfumo huo itakuwa imekiuka matakwa ya Sheria ya Ununuzi wa Umma.

"Serikali itaendelea kusimamia matumizi ya Mfumo wa NeST ili kuhakikisha taasisi zote za umma zinafuata sheria na taratibu zilizowekwa," alisema Dkt. Nguvila.

Aidha, Dkt. Nguvila aliipongeza Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) kwa kuendelea kusimamia utekelezaji wa Sheria ya Ununuzi wa Umma na kuimarisha matumizi ya Mfumo wa NeST, ambapo aliitaka Mamlaka hiyo kuendelea kuuboresha Mfumo huo na kuuunganisha na mifumo mingine ya Serikali ili kuongeza ufanisi, kurahisisha ubadilishanaji wa taarifa na kuimarisha usimamizi wa matumizi ya fedha za umma.

Aliongeza kuwa Serikali inaendelea kutambua ununuzi wa umma kama nyenzo muhimu ya sera ya uchumi inayochochea maendeleo ya viwanda vya ndani, kukuza ushiriki wa wazabuni wazawa, kuongeza ajira na kuchangia ukuaji wa uchumi wa Taifa pamoja na kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Bw. Dennis Simba, alisema taasisi zote za Serikali zinapaswa kuzingatia kikamilifu Sheria ya Ununuzi wa Umma, akisisitiza kuwa taasisi zitakazoshindwa kutekeleza matakwa ya sheria hiyo zitawekwa hadharani, ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo ya, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Bw. Simba pia aliwapongeza wadau walioshiriki Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma 2026 na kuwataka kutumia fursa hiyo kuongeza uelewa na uwezo wa kitaalamu ili kuendelea kuboresha utekelezaji wa shughuli za ununuzi wa umma nchini.

Katibu Tawala Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila (kushoto), akipata maelezo kuhusu Sera ya Ununuzi wa Umma, kutoka kwa Afisa Ugavi Mwandamizi Idara ya Sera za Ununuzi wa Umma Wizara ya Fedha, Bw. Richard Benaya, alipotembelea Banda la Wizara ya Fedha wakati wa Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma 2026, linalofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC). Kushoto ni Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Bw. Dennis Simba

Katibu Tawala Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila (kushoto), akiagana na  Afisa Ugavi Mwandamizi Idara ya Sera za Ununuzi wa Umma Wizara ya Fedha, Bw. Richard Benaya, baada ya kutembelea Banda la Wizara ya Fedha wakati wa Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma 2026, linalofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).

Katibu Tawala Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila, akiitaka Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) kuhakikisha Mfumo wa Kielektroniki wa Ununuzi wa Umma (NeST) unasomana na Mifumo mingine Serikalini ili kurahisisha utendaji, wakati wa Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma 2026, linalofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).

Kamishana Idara ya Sera za Ununuzi wa Umma Bw. Alex Haraba, akifuatilia maelezo ya Katibu Tawala Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila, wakati wa Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma 2026, linalofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).

Mkurugenzi wa Kitengo cha Ununuzi, Wizara ya Fedha, Bw. Boaz Ntembanda akifuatilia maelezo ya Katibu Tawala Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila, wakati wa Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma 2026, linalofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).


Afisa Ugavi Mwandamizi Idara ya Sera za Ununuzi wa Umma, Wizara ya Fedha, Bi. Jamila Byekwaso, akitoa elimumu ya Sera  za Ununuzi wa Umma, kwa wadau wa Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma 2026, linalofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).

Baadhi ya Maafisa wa Idara ya Sera za Ununuzi wa Umma, Wizara ya Fedha, wakiwa katika picha ya pamoja wakati wa Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma 2026, linalofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).

Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma 2026, linalofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).

 

 (Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha, Arusha)


Na. Ramadhani Kissimba, Durban.


Nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) zimeshauriwa kuwekeza zaidi katika maendeleo ya viwanda na miundombinu ili kuwawezesha wanawake na vijana kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji na kuongeza mchango wao katika ukuaji wa uchumi wa ukanda wa SADC.

Ushauri huo umetolewa jijini Durban nchini Afrika Kusini na Meneja wa Utafiti na Biashara wa Benki ya Maendeleo Tanzania (TIB), Dkt. Hilderbrand Shayo, kando ya Mkutano wa Wiki ya Viwanda wa SADC unaoendelea nchini humo.

Alisema kuwa uwekezaji katika viwanda vya kuongeza thamani ya bidhaa utasaidia kuwainua wanawake na vijana kiuchumi, kupanua masoko ya bidhaa za Tanzania na kuongeza mapato yatokanayo na mauzo ya bidhaa nje ya nchi.

Akizungumzia kuhusu ushiriki wa Tanzania katika mkutano na maonesho hayo, Dkt. Shayo alisema matukio hayo yanaendana na vipaumbele vya maendeleo vya Tanzania, hususan katika sekta za madini, kilimo, bidhaa za afya pamoja na maendeleo ya miundombinu na ubunifu, ambazo ni maeneo yanayopewa kipaumbele katika kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

"Ushiriki wa Tanzania katika Wiki ya Viwanda ya SADC una umuhimu mkubwa kwa sababu mkutano huu umejikita katika kuimarisha mnyororo wa thamani wa sekta za madini, kilimo na bidhaa za afya, sambamba na maendeleo ya miundombinu na ubunifu na ni maeneo muhimu katika safari ya Tanzania kuelekea uchumi wa viwanda na maendeleo endelevu," alisema Dkt. Shayo.

Aidha, alisema kuwa maonesho hayo yamefungua fursa mpya za uwekezaji, ambapo wawekezaji kutoka nchi mbalimbali wameonesha nia ya kuwekeza nchini Tanzania kutokana na mazingira mazuri ya biashara pamoja na nafasi ya kimkakati ya nchi hiyo kama lango la biashara kupitia Bandari ya Dar es Salaam inayohudumia nchi nyingi wanachama wa SADC.

Dkt. Shayo, aliongeza kuwa ushiriki wa Tanzania katika maonesho hayo umeiwezesha nchi kuzitangaza fursa zake za uwekezaji na kuimarisha ushirikiano wa kibiashara na wadau mbalimbali wa maendeleo kutoka ndani na nje ya ukanda wa SADC.

Sambamba na hilo, Dkt. Shayo alizishauri taasisi za fedha zilizoshiriki katika mkutano huo, ikiwemo Benki ya Maendeleo Tanzania (TIB), Benki ya Exim, BADEA, Nedbank na taasisi nyingine za kifedha, kuimarisha ushirikiano katika kutafuta mitaji na fedha za kugharamia miradi ya maendeleo na uwekezaji nchini Tanzania.

"Taasisi za fedha zilizoshiriki katika maonesho haya zina nafasi kubwa ya kushirikiana katika kuhamasisha upatikanaji wa fedha kwa ajili ya miradi ya maendeleo na uwekezaji ambayo itachochea ukuaji wa uchumi wa Tanzania," alisema Dkt. Shayo

Akizungumzia sekta ya madini, Dkt. Shayo alisema Tanzania imebarikiwa kuwa na madini mengi ya kimkakati yanayohitajika duniani, hususan katika kipindi hiki cha maendeleo ya teknolojia.

Alisisitiza umuhimu wa kuyachakata madini hayo ndani ya nchi badala ya kuuza malighafi pekee, hatua ambayo itaongeza thamani ya bidhaa, kuzalisha ajira zaidi, kuongeza mapato ya fedha za kigeni na kuchochea ukuaji wa viwanda vya ndani.

Mkutano wa Wiki ya Viwanda wa SADC umeendelea kuwa jukwaa muhimu la kuimarisha ushirikiano wa kikanda katika biashara, uwekezaji na maendeleo ya viwanda. Kwa Tanzania, ushiriki katika mkutano huo unaendelea kufungua fursa mpya za uwekezaji, masoko na ubia wa kifedha, huku ukiunga mkono juhudi za Serikali za kujenga uchumi wa viwanda, kuongeza thamani ya rasilimali za ndani na kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.


Baadhi ya Washiriki wa Wiki ya Tisa ya Viwanda kutoka nchi wanachama wa SADC wakifuatilia mojawapo ya mjadala kuhusu masuala ya madini uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (ICC), Durban, Afrika Kusini.

Meneja wa Mawasiliano, Masoko na Mahusiano wa Benki ya Maendeleo - TIB, Bw. Allan Chonjo akitoa maelezo kuhusu bidhaa na huduma zinazotolewa na Benki hiyo kwa baadhi ya wadau waliotembelea Banda la Tanzania, pembezoni mwa Mkutano wa Wiki ya Viwanda ya SADC (SADC Industrialisation Week 2026) unaofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (ICC), jijini Durban, Afrika Kusini.

Afisa Sheria kutoka Tume ya Ushindani (FCC) akielezea ubora na faida za mkonge unaozalishwa Tanzania kwa mdau aliotembelea Banda la Tanzania, pembezoni mwa Mkutano wa Wiki ya Viwanda ya SADC (SADC Industrialisation Week 2026) unaofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (ICC), jijini Durban, Afrika Kusini.

Baadhi ya Washiriki kutoka Wizara na Taasisi mbalimbali wakiwa katika picha ya Pamoja baada ya Mkutano wa Wiki ya Viwanda ya SADC (SADC Industrialisation Week 2026) unaofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (ICC), jijini Durban, Afrika Kusini.


Katika kuendeleza dhamira yake ya kuchangia maendeleo ya jamii kupitia mpango wa Uwajibikaji kwa Jamii (CSI) chini ya kampeni yake ya #PSSSFKaribuNaJamii, Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) umekabidhi rasmi mradi wa miundombinu wenye thamani ya Shilingi milioni 25 katika Shule ya Msingi Majani Mapana iliyopo mkoani Tanga.

Mradi huo unahusisha ujenzi wa chumba cha darasa, chumba cha mapumziko pamoja na vifaa mbalimbali vya michezo kwa ajili ya watoto wenye mahitaji maalum.

Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Bw. Kwame Temu alieleza kuwa msaada huo unalenga kuunga mkono juhudi za Serikali kwa kuhakikisha watoto wenye mahitaji maalum wanapata haki yao ya msingi ya elimu. Alisisitiza kuwa hatua hiyo itawasaidia wanafunzi hao kujifunza katika mazingira yanayowawezesha kujifunza kwa ufanisi, kushiriki katika michezo na kukuza vipaji vyao mbalimbali.

Kwa upande wake, Afisa Elimu Kata ya Nguvumali, Bi. Lilian Shetui, aliishukuru PSSSF kwa mchango huo akieleza kuwa miundombinu hiyo itaongeza ubora wa huduma za elimu shuleni hapo. Kwa niaba ya Afisa Elimu Shule za Awali na Msingi wa mkoa huo, Bi. Lilian alipongeza PSSSF kwa kuona umuhimu wa kundi hilo na kutoa msaada utakaokuwa na tija kubwa kwa watoto hao.

Kupitia mchango huo, jumla ya wanafunzi 71 wenye mahitaji maalum na usonji katika Shule ya Majani Mapana wanatarajiwa kunufaika na mazingira rafiki ya kujifunzia, kupumzika na kucheza, hatua inayochochea elimu jumuishi na kuwajengea msingi bora wa maisha ya baadaye.



Na Vero Ignatus, Arusha

Mkutano Mkuu wa Tano wa Chama cha Wataalamu wa Ununuzi na Ugavi Tanzania (APSP) umefanyika jijini Arusha ukiwa na lengo la kupokea taarifa za uongozi, kujadili utekelezaji wa maazimio, fedha na bajeti, pamoja na kuweka mikakati ya kuongeza ushiriki wa makundi maalum na biashara ndogo na za kati (SMEs) katika fursa za ununuzi wa umma.

Akifungua mkutano huo, Mlezi wa APSP na Kamishna Mstaafu wa Sera za Ununuzi wa Umma, Dkt. Fredrick Asumile Mwakimbinga, alisema zaidi ya asilimia 70 ya fedha za Serikali hupitia katika shughuli za ununuzi, hivyo aliwataka wataalamu wa sekta hiyo kufanya kazi kwa uadilifu, kuzingatia maadili ya taaluma na kulinda heshima ya taasisi zao.

Dkt. Mwakimbinga pia aliwahimiza wanachama kuendelea kuimarisha taaluma ya ununuzi na ugavi kwa kuzingatia sheria na matumizi ya teknolojia, kushiriki kutoa elimu kwa umma, kusimamia migogoro ya mikataba, kufanya ukaguzi wa bidhaa na kuzuia bidhaa bandia ili kuhakikisha fedha za umma zinatumika kwa ufanisi na miradi ya maendeleo inatekelezwa kwa wakati.

Alisema kaulimbiu ya mkutano huo, inayohusu kuimarisha ushiriki wa kitaaluma na kuwezesha makundi maalum pamoja na SMEs kunufaika na fursa za ununuzi wa umma, inalenga kuwafanya wataalamu kuwa kiungo muhimu kati ya sheria, urasimishaji wa biashara na utekelezaji wa maendeleo nchini.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya APSP, Dkt. Emmanuel Urembo, alisema mustakabali wa taaluma hiyo unategemea uwezo wa wataalamu kuendana na maendeleo ya teknolojia, kuzingatia maadili na kutoa ushauri wa kimkakati. Alibainisha kuwa chama kina wanachama zaidi ya 2,200 na kimepata mafanikio ikiwemo kusaini mikataba ya ushirikiano, kulipa deni la kiwanja la shilingi milioni 134 na kusajili nembo ya chama kupitia BRELA.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Huduma za Sheria na Uzingatiaji kutoka BRELA, Wakili Lamecky Nyangi Samson, alisema wataalamu wa ununuzi wana mchango mkubwa katika kuhamasisha urasimishaji wa biashara kwa kuzingatia sheria na kuunganisha wafanyabiashara na fursa zinazotokana na ununuzi wa umma.

Akifunga mkutano huo, Mkurugenzi Mkuu wa PPRA, Bw. Denis Kwame Simba, aliwataka washiriki kutumia mifumo ya kielektroniki kwa ufanisi, kuzingatia uwazi, ushindani na thamani ya fedha, kutenga asilimia 30 ya zabuni kwa makundi maalum, kusimamia vihatarishi, kujibu hoja za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa wakati na kuzingatia masuala ya mabadiliko ya tabianchi katika utekelezaji wa shughuli za ununuzi wa umma.
Mlezi wa APSP na Kamishna Mstaafu wa Sera za Ununuzi wa Umma, Dkt. Fredrick Asumile Mwakimbinga,




Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) inapenda kuwataarifu wadau wote kuwa muda wa kuwasilisha Expression of Interest (EOI) kwa ajili ya uwekezaji kwenye ardhi zinazomilikiwa na TBA kupitia mfumo wa Public-Private Partnership (PPP) umeongezwa.

Hii ni fursa kwa wawekezaji wenye sifa kuandaa na kuwasilisha maombi yao ndani ya muda mpya uliotangazwa.






Na. Mwandishi wetu, Sumbawanga
WADAU wa maendeleo ndani na nje ya mkoa wa Rukwa wamehamasishwa kuchangia upatikanaji wa madawati kwa ajili ya kuwezesha watoto kusoma kwenye mazingira wezeshi kwa ustawi wa taaluma.

Wito huo umetolewa hivi karibuni na Mbunge wa Jimbo la Kwela ambaye pia ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu wakati alipokabidhi madawati kwa shule za msingi katika jimbo hilo alipofanya ziara ya kikazi.

Katika ziara hiyo sangu alikabidhi madawati zaidi ya 100 kwa shule za msingi sita (6) yenye thamani ya shilingi Milioni 60 ambayo ameyapata kupitia ufadhili ya Benki ya Taifa ya Biashara (NBC).

Waziri Sangu akizungumza kwenye moja ya mikutano yake na wananchi wa kijiji cha Nankanga tarafa ya Kipeta na kijiji cha Ilemba alisema ametoa msaada huo kuunga mkono jitihanda za wananchi katika kuchangia maendeleo ya elimu.

“ Nimekuja hapa kukabidhi zawadi ndogo kwa Watoto.Leo nimewaletea madawati 20 ambapo yatasaidia Watoto 60 kutoendelea kukaa chini” alisema Waziri Sangu.

Mbunge huyo aliongeza kuwaambia wananchi kuwa yeye ni mbunge wa vitendo na kwamba anapenda vitu vinavyoonekana ambapo aliitumia fursa hiyo kushukuru uongozi wa Benki ya NBC kwa kuguswa na shida za wanaKwela .

“Ninashukuru benki ya NBC kwa msaada wao waliotupatia madawati haya yanayokwenda kupunguza tatizo la watoto kukaa chini. utatuzi huu wa kero za wananchi ni sehemu ya maelekezo tuliyopewa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwetu wabunge” alisema Sangu alipoongea na wananchi wa Kijiji cha Msia kata ya Milepa huku akitoa wito kwa wadau wengine wa maendeleo kuchangia madawati kwa ajili ya jimbo la Kwela.

Miongoni mwa shule zilizopokea madawati hayo na idadi yake kwenye mabano ni shule ya msingi Kalumbaleza (20), Msia (20), Kimambo (15), Ilemba (20) , Nankanga (20) na Deusi Sangu sekondari madawati (30).

Akizungumza kwa niaba ya wananchi, Diwani wa kata ya Mwadui Mahmood Leonce Mgweno alisema amepokea madawati toka Ofisi ya Mbunge na kwa tayari amefikisha shuleni na kumpongeza Mbunge Sangu kwa msaada.

Nao wananchi wametumia fursa ya ziara ya mbunge Sangu kueleza kufurahishwa kwao na jitihada anazozifanya kuchangia maendeleo ya jimbo hilo ikiwemo msaada wa madawati.

Nae Bwa.Thomas Nsandale ameishukuru Ofisi ya Mbunge kwa kuwezesha wa upatikanaji wa madawati ikiwa ni miongoni mwa vingi walivyopatiwa katika kipindi chote Mhe.Sangu akiwa Mbunge wa Jimbo la Kwela

“Sangu amefanya mambo mengi ambayo yanatufanya sisi wananchi kutokupunguza upendo juu yake na tunamuomba pia Madawati haya yasiwe ya mwisho kwa wananchi wake wa Kwela Bali iwe sababu ya muendelezo wa Maendeleo haya” amesema Nsandale.

Waziri Sangu alikuwa jimboni Kwela wilaya ya Sumbawanga kukagua shughuli za maendeleo pamoja na kuzungumza na wananchi.
Na Mwandishi Wetu
BODI  ya Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC), ikiongozwa na Mwenyekiti wake, Prof. Joseph Msambichaka, imefanya ziara ya kikazi katika Bandari ya Dar es Salaam na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere (JNIA) kujionea utekelezaji wa usimamizi wa matumizi salama ya mionzi katika vifaa vya ukaguzi wa mizigo vinavyotumia teknolojia ya skana.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Prof. Msambichaka amesema Bodi imeridhishwa na kiwango cha uzingatiaji wa usalama wa mionzi pamoja na ufanisi wa matumizi ya skana katika ukaguzi wa makasha na mizigo. Amesema TAEC ina jukumu la kusimamia matumizi salama ya vifaa vinavyotumia mionzi kupitia utoaji wa leseni, ukaguzi wa mara kwa mara na mafunzo kwa watumiaji wa vifaa hivyo, ili kuhakikisha usalama wa wafanyakazi, madereva na wananchi kwa ujumla.

“Tumekuja kujionea kazi inayofanywa na TAEC katika kusimamia matumizi salama ya mionzi kwenye skana zinazotumika bandarini. Tumejiridhisha kuwa mazingira ya kazi ni salama kwa wafanyakazi, madereva na wananchi kwa ujumla,”amesema

amesema Prof. Msambichaka. Ameongeza kuwa matumizi ya teknolojia ya skana yameongeza ufanisi wa huduma bandarini kwa kupunguza muda wa ukaguzi wa makasha, kuimarisha usalama wa biashara na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa. Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Huduma za Usalama wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), Dkt. Jumanne Fhika, amesema Bandari ya Dar es Salaam kwa sasa inatumia mashine 11 za skana ambazo zimeongeza kasi na ufanisi wa ukaguzi wa mizigo, kupunguza muda wa kuhudumia makasha na kuchangia ongezeko la mapato ya Serikali. Katika kuendelea na ziara hiyo, wajumbe wa Bodi ya TAEC walitembelea eneo la ukaguzi wa mizigo katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere (JNIA), ambapo walijionea namna TAEC inavyosimamia na kudhibiti matumizi ya vifaa vya mionzi vinavyotumika kukagua mizigo inayoingia na kutoka nchini. Ziara hiyo ililenga kujiridhisha kuwa matumizi ya teknolojia ya mionzi katika ukaguzi wa mizigo yanafanyika kwa kuzingatia viwango vya usalama ili kulinda wananchi, wafanyakazi na mazingira dhidi ya athari zinazoweza kusababishwa na mionzi.

Aidha, Bodi hiyo ilitembelea Kituo cha Kitaifa cha Ufuatiliaji wa Mionzi na Uchafuzi wa Anga, kinachosimamia utekelezaji wa Mkataba wa Kupiga Marufuku Majaribio ya Silaha za Nyuklia (Comprehensive Nuclear-Test-Ban Treaty Organization – CTBTO).

Akitoa maelezo katika kituo hicho, Mkurugenzi Mkuu wa TAEC, Prof. Najat Kassim Mohammed, amesema Tanzania inaendelea kutekeleza kikamilifu wajibu wake wa kimataifa kwa kushiriki katika utekelezaji wa Mkataba wa Kupiga Marufuku Majaribio ya Silaha za Nyuklia, ikiwa ni miongoni mwa nchi zilizouridhia mkataba huo.

Prof. Najat amesema kituo hicho kina jukumu muhimu la kufuatilia na kupima viashiria vya mionzi na uchafuzi wa anga, hatua inayochangia kuimarisha usalama wa taifa, kulinda mazingira na kutekeleza wajibu wa Tanzania katika mfumo wa kimataifa wa ufuatiliaji wa majaribio ya nyuklia. Ziara hiyo imeiwezesha Bodi ya TAEC kujionea kwa karibu utekelezaji wa majukumu ya Tume katika maeneo muhimu ya kimkakati, yakiwemo usimamizi wa matumizi salama ya mionzi, ulinzi wa wananchi na mazingira, pamoja na matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika kuimarisha usalama na kuchochea maendeleo ya uchumi wa Taifa.






Na Mwandishi Wetu, Busan, Korea Kusini
KIONGOZI wa jadi wa Kimasai, Isack Lekisongo Meijo, ametoa wito wa kuwepo kwa uwiano endelevu kati ya binadamu, mifugo na wanyamapori katika Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro ili kulinda urithi huo wa dunia na kuhakikisha maendeleo endelevu ya jamii za wafugaji.

Meijo alitoa kauli hiyo wakati wa mjadala uliofanyika sambamba na Kikao cha 48 cha Kamati ya Urithi wa Dunia cha UNESCO kilichofanyika Busan, Jamhuri ya Korea, ambapo Tanzania iliwasilisha taarifa kuhusu matokeo ya Tume mbili za Rais zilizochunguza masuala ya ardhi na uhamaji wa hiari wa wananchi kutoka Ngorongoro.

Alisema kwa vizazi vingi jamii ya Wamasai imeishi sambamba na wanyamapori huku ikichangia kuhifadhi mfumo wa ikolojia wa Ngorongoro, akisisitiza kuwa hakuna Ngorongoro bila Wamasai na hakuna Ngorongoro bila wanyamapori.

Akifafanua changamoto iliyopo, Meijo alifananisha Ngorongoro na ndege inayobeba wafugaji, mifugo na wanyamapori, akisema mzigo umeongezeka kupita uwezo wa eneo hilo. Alieleza kuwa ili safari iwe salama na endelevu, ni lazima kupunguza shinikizo kwa njia iliyopangwa na yenye uwiano.

Alisema ongezeko la watu, makazi, mifugo na wanyamapori ndani ya eneo lisiloongezeka ukubwa wake limeifanya mfumo wa matumizi mchanganyiko ya ardhi kukabiliwa na changamoto kubwa za uendelevu. Kwa mujibu wake, baadhi ya wadau wanaunga mkono uhamaji wa hiari wa wafugaji kwenda maeneo yenye fursa zaidi za kijamii na kiuchumi, huku wengine wakipendekeza kuhamisha wanyamapori ili kupunguza shinikizo kwa mazingira.

Meijo alisisitiza kuwa lengo kuu ni kulinda thamani ya kipekee ya Ngorongoro kama Urithi wa Dunia huku ukiimarisha maisha ya sasa na ya baadaye ya jamii ya Wamasai. Pia aliahidi kuwa jamii hiyo itaendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania, UNESCO pamoja na wadau wengine kuhakikisha uhifadhi, utamaduni na maendeleo endelevu vinaenda sambamba.

Katika mjadala huo, mjumbe kutoka Zimbabwe alihoji ni ipi kati ya kuhamisha wafugaji au kuhamisha wanyamapori inayobeba hatari kubwa zaidi. Akijibu kwa niaba ya Serikali ya Tanzania, Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO Tanzania, Profesa Hamisi Malebo, alisema kuwa uhamaji wa hiari wa wananchi ni rahisi zaidi kuliko kuhamisha wanyamapori, jambo ambalo lina changamoto kubwa za kitaalamu, kifedha na kimazingira.

Washiriki kutoka mataifa 36 waliipongeza Tanzania kwa kuandaa mjadala huo, wakikubaliana kuwa ongezeko la watu, mifugo, migongano kati ya binadamu na wanyamapori pamoja na mabadiliko ya tabianchi vimeongeza shinikizo katika Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro na kwamba hatua za pamoja zinahitajika kulinda urithi huo wa dunia.

MAHAKAMA ya Wilaya ya Mkinga mkoani Tanga imemuhukumu Isa Musini Rashidi  maarufu kama Hamidu kifungo cha miaka 30 jela baada ya kupatikana na htia ya kosa la kusafirisha kilo 75.15 za dawa za kulevya aina ya mirungi.

Hukumu hiyo imesomwa hivi karibuni na Hakimu Mkazi Azizi Khamis, baada ya Mahakama kuridhika na ushahidi uliotolewa na upande wa mashtaka ambao uliweza kuthibitisha shtaka dhidi ya mshtakiwa bila kuacha shaka yoyote ya msingi.

Akisoma hukumu hiyo, Hakimu Khamis alisema mahakama imeridhaka na ushahidi uliowasilishwa na upande wa mashtaka na vielelezo ambapo wameweza kuthibitisha pasipo kuacha shaka yoyote kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo.

"Mahakama hii inakutia hatiani kwa kosa la kusafirisha dawa za kulevya kinyume cha Kifungu cha 16(1) na (2)(c) cha Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, Sura ya 95, Marejeo ya Mwaka 2023, na inakuhukumu kifungo cha miaka 30 jela" alisema Hakimu Khamis.

Awali mahakamani hapo ilielezwa kuwa Aprili 10, 2026, katika eneo la Kinyatu ‘A’, Wilaya ya Mkinga mkoani Tanga, maafisa wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) walimkamata Isa akiwa anaendesha pikipiki nyeusi aina ya Huoniao yenye namba za usajili MC 569 EYG, akiwa amebeba mifuko miwili iliyokuwa na jumla ya mafungu 122 ya majani yaliyodhaniwa kuwa mirungi.

Uchunguzi wa kitaalamu uliofanywa na Mkemia Mkuu wa Serikali ulithibitisha kuwa majani hayo yalikuwa mirungi yenye uzito wa kilo 75.15.

Katika kuthibitisha shtaka, upande wa mashtaka uliwasilisha mashahidi watano na vielelezo kumi huku mshtakiwa akikana tuhuma zilizokuwa zikimkabili.

Baada ya kuchambua ushahidi uliowasilishwa na pande zote, Mahakama iliridhika kuwa ushahidi wa upande wa mashtaka ulikuwa thabiti na uliweza kuthibitisha kuwa mshtakiwa alikamatwa akiwa anasafirisha mirungi hiyo.

Mahakama pia iliridhika kuwa vielelezo vilihifadhiwa na kushughulikiwa kwa kufuata taratibu, kuanzia wakati wa ukamataji, uchunguzi wa kitaalamu hadi kuharibiwa kwa mujibu wa amri ya Mahakama.

Aidha, Mahakama imeamuru pikipiki aina ya Huoniao yenye namba za usajili MC 569 EYG, iliyotumika kusafirisha dawa hizo, itaifishwe na kuuzwa kwa mnada wa hadhara.

Na Mwandishi wetu, Arusha

Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imeshiriki Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma mwaka 2026 linaloendelea jijini Arusha, limewakutanisha wadau wa ununuzi pamoja na viongozi wa Serikali kwa lengo la kujadili na kuweka mikakati ya kuimarisha Sekta ya ununuzi na ugavi nchini.

Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando, Mkuu wa Sehemu ya Huduma za Sheria PPAA, Bi. Agnes Sayi amewahimiza wadau wa ununuzi wa umma kutembelea banda la Mamlaka ya Rufani kupata uelewa juu ya majukumu na huduma mbalimbali zinazotolewa na taasisi hiyo hususan matumizi ya Moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST.

PPAA imeshiriki maonesho yanayofanyika pembezoni mwa Kongamano hilo kwa lengo la kutoa elimu kuhusu uamuzi juu ya rufaa zinazotokana na mchakato wa ununuzi wa umma, uamuzi juu ya rufaa zinazotokana na kufungiwa kushiriki katika michakato ya ununuzi wa umma pamoja na uamuzi juu ya malalamiko yanayotokana na kushindwa kwa Afisa Masuuli kutoa uamuzi ndani ya muda uliowekwa.

Awali, akifungua Kongamano hilo kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar, (Mb.), Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila amesema sekta ya ununuzi wa umma inahusisha sehemu kubwa ya matumizi ya fedha za serikali, hivyo kuna ulazima wa kuhakikisha fedha zote zinazotengwa zinasimamiwa kwa umakini mkubwa ili kuleta matokeo yaliyokusudiwa.

Dkt. Nguvila amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuimarisha matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika mfumo wa ununuzi wa umma ili kuongeza uwazi, kupunguza gharama za ununuzi, kuharakisha mchakato na kurahisisha ufuatiliaji wa matumizi ya fedha za umma.

"Ununuzi wa umma na ugavi ni nyenzo ya kisera na kimkakati ya Serikali katika kuchochea uzalishaji, ukuaji wa viwanda, kuongeza ajira, kuimarisha kampuni za ndani, kukuza ubunifu, na kuhakikisha maendeleo yanayopatikana yanawanufaisha Watanzania wengi zaidi," amesema Dkt. Nguvila.

Kongamano hilo la siku tatu limeanza tarehe 29 - 31 Julai, 2026 limewakutanisha wadau wa ununuzi zaidi ya 1,500. Aidha, limewakutanisha Wakuu wa Taasisi, Maafisa Masuuli, Maafisa Ununuzi, Idara Tumizi, Maafisa Sheria, Wazabuni na Taasisi binafsi. 





 


Mwandishi Wetu, Dar es Salaam, Julai 29, 2026

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imeanza rasmi kutoa mafunzo kwa waandishi wa habari nchini, yakilenga kuimarisha weledi, maadili na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo kwa waandishi wa habari wa Bongo FM jijini Dar es Salaam, redio dada ya Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), kwa niaba ya Mwenyekiti wa Bodi ya JAB, Tido Mhando, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, amesema mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo wa kuelewa na kutekeleza matakwa ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, kwa kuzingatia weledi, maadili na uwajibikaji.

“Mafunzo haya ni utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari. Leo tumeanza rasmi na waandishi wa habari wa Bongo FM, tutaendelea kwa vyombo vingine pia kwa sababu, kutakuwa na mafunzo ya muda mfupi na ya muda mrefu. Hivyo, mafunzo haya yawe fursa ya kujenga uwezo na kuweka msingi imara wa kukuza na kulinda taaluma ya uandishi wa habari kwa kuongeza maarifa na weledi,” amesema Wakili Kipangula.

Akiwasilisha mada kuhusu Sheria ya Huduma za Habari, historia na uanzishwaji wake, katika mafunzo hayo yaliyoanza leo tarehe 29 Julai, 2026 katika ukumbi wa Bodi, Wakili Kipangula amesema sheria hiyo imeweka msingi wa kuimarisha taaluma ya habari kwa kubainisha viwango vya weledi, maadili na uwajibikaji.

Amesisitiza kuwa JAB itaendelea kusimamia utekelezaji wa sheria hiyo kwa kuzingatia haki, uwazi na kuheshimu uhuru wa vyombo vya habari, huku ikihakikisha taaluma ya habari inalinda maslahi ya umma..

Aidha, amewataka waandishi wa habari kuzingatia sheria na maadili katika kila hatua ya ukusanyaji, uchakataji na usambazaji wa habari ili kujiepusha na madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na ukiukaji wa taaluma.

Amesema kuzingatia misingi hiyo kunajenga weledi, kunalinda heshima ya taaluma na kuimarisha imani ya jamii kwa vyombo vya habari.

Kwa upande wake, Dkt. Egbert Mkoko, akiwasilisha mada kuhusu Maadili ya Uandishi wa Habari, amesema maadili ni nguzo muhimu ya taaluma inayojengwa katika misingi ya ukweli, usahihi, haki, mizania, uwajibikaji na kutanguliza maslahi ya umma.

Amesisitiza kuwa mwandishi wa habari hapaswi kuongozwa na kasi ya kuwahi kuripoti habari, shinikizo la mitandao ya kijamii, umaarufu au maslahi binafsi, bali na ukweli na uwajibikaji.

Baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo, akiwemo Bi. Irene Kilango na Bw. Anord Philemon, wameishukuru JAB kwa kuandaa mafunzo hayo, wakisema yamewaongezea uelewa kuhusu Sheria ya Huduma za Habari, maadili ya taaluma na wajibu wa mwandishi wa habari katika kutekeleza majukumu yake kwa weledi.

"Mafunzo haya yametupatia maarifa muhimu yatakayotusaidia kutekeleza majukumu yetu kwa kuzingatia maadili, sheria na viwango vya taaluma ya uandishi wa habari. Tunaamini yatachangia kuboresha utendaji wetu na kuongeza uwajibikaji katika kuhabarisha umma," wamesema washiriki hao.

Mafunzo hayo ni sehemu ya mpango endelevu wa JAB wa kuwajengea uwezo waandishi wa habari nchini ili kuhakikisha wanazingatia Sheria ya Huduma za Habari, maadili, weledi na viwango vya taaluma katika utekelezaji wa majukumu yao, kwa lengo la kuimarisha ubora wa huduma za habari na kulinda maslahi ya umma.





Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Maonesho ya 88 ya Kitaifa ya Kilimo, Ufugaji na Uvuvi yanayotarajiwa kufungukiwa tarehe mosi  Agosti, jijini Dodoma mwaka 2026 yameweka rekodi mpya ya ushiriki wa waonyeshaji 1,133, ikiwa ni ongezeko la asilimia 26 ikilinganishwa na maonesho ya mwaka uliopita.

Washiriki hao ni pamoja na waonyeshaji 24 kutoka mataifa mbalimbali na wajasiriamali wadogo 20, hatua inayoonyesha kuendelea kukua kwa maonesho hayo na kuvutia wadau wengi wa sekta za kilimo, ufugaji na uvuvi kutoka ndani na nje ya Tanzania.

Akizungumza leo katika Viwanja vya Maonesho vya Nzuguni baada ya kukagua maandalizi ya maonesho hayo, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, amesema maandalizi yote yamekamilika na Dodoma ipo tayari kuwa mwenyeji wa maonesho hayo ya kitaifa na kimataifa.

Amesema washiriki wote wamejipanga kutoa elimu, kuonesha teknolojia za kisasa pamoja na bidhaa mbalimbali zinazohusu kilimo, uvuvi na ufugaji ili kuwawezesha wananchi kujifunza mbinu bora za kuongeza tija katika uzalishaji.

"Maonesho ya mwaka huu yamepata mwitikio mkubwa zaidi kuliko mwaka uliopita. Waonyeshaji wameongezeka kwa asilimia 26 na kufikia 1,133, jambo ambalo ni rekodi katika historia ya Viwanja vya Maonesho vya Nzuguni," amesema Senyamule.

Amewataka wananchi kutoka mikoa mbalimbali kujitokeza kutembelea maonesho hayo ili kunufaika na elimu, huduma na fursa mbalimbali zinazotolewa na taasisi za Serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo katika eneo moja.

Aidha, amesema miundombinu ya Viwanja vya Nzuguni imeendelea kuboreshwa kwa kujengwa majengo ya kisasa na ya kudumu pamoja na maeneo ya makongamano, hatua itakayowezesha uwanja huo kutumika kwa shughuli mbalimbali za kiuchumi na kijamii mwaka mzima, hata baada ya maonesho kumalizika.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Mhandisi Athumani Kilundumya, amewahamasisha Watanzania kutembelea Maonesho ya 88 ya Kitaifa pamoja na maonesho yanayofanyika katika kanda zote nane ili kujifunza teknolojia zitakazowasaidia kubadili kilimo cha mazoea na kuwa kilimo cha biashara.

Amesema matumizi ya mbegu bora bado ni changamoto kwa wakulima wengi nchini, hivyo maonesho hayo yamekusanya wataalamu mbalimbali watakaotoa elimu kuhusu mbegu bora, teknolojia za kisasa na mbinu za kuongeza uzalishaji katika sekta za kilimo, uvuvi na ufugaji.

Maonesho ya 88 Kitaifa mwaka 2026 yanatarajiwa kushirikisha wadau kutoka mataifa mbalimbali duniani, ikiwemo China, Israel, Urusi, Japan, Saudi Arabia, Sweden na nchi nyingine, huku yakitarajiwa kuwa jukwaa muhimu la kubadilishana uzoefu, teknolojia, uwekezaji na fursa za biashara katika sekta za kilimo, ufugaji na uvuvi.









 Mkuu wa mkoa wa Iringa Komred Kheri James,mapema leo amekutana na kufanya mazungumzo na viongozi wa Jumuiya za Wazee mkoani humo,lengo likiwa ni kupokea ushauri,Taarifa ya hali ya Jumuiya hizo pamoja na kushauriana juu ya masuala muhimu yanayo gusa mkoa wa Iringa.         

Akizungumza katika kikao hicho  Komred Kheri James amewashukuru Wazee wa mkoa wa Iringa kwa ushirikiano wao, busara,ushauri na ushiriki wao katika kujenga umoja,kusimamia maadili,kutoa ushauri na uzoefu,pamoja na utatuzi wa migogoro ya kijamii.                             

Aidha Komred Kheri James amewahakikishia Wazee wa mkoa wa Iringa dhamira ya Serikali kuendelea Kusimamia ustawi wa wazee,huduma kwa Wazee na kushirikiana na Jumuiya za Wazee zilizopo katika kuwahudumia na kusimamia maslahi na hoja za Wazee zinazo wasilishwa na kusimamiwa na Jumuiya hizo.










Top News