Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
Viongozi wapya wa Chama cha Waandishi Waendesha Ofisi Tanzania (TAPSEA) wameapishwa rasmi jijini Dar es Salaam, huku wakitakiwa kusimamia Katiba ya chama na kulinda maslahi ya wanachama katika utekelezaji wa majukumu yao.
Akizungumza wakati wa kuwaapisha viongozi hao, Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Franco Kiswaga, aliwataka kuzingatia Katiba ya TAPSEA na kuitumia kama mwongozo katika uongozi wao ili kuhakikisha wanachama wanaongozwa kwa haki na ufanisi.
Kiswaga amesema TAPSEA ni chama kikubwa chenye wajibu wa kuwatumikia wanachama wake, hivyo viongozi wanapaswa kuwa imara katika kusimamia maslahi yao na kuhakikisha chama kinaendelea kusonga mbele.
“Niwaombe viongozi mnapotoka hapa mkasimamie vyema Katiba yenu ili kuweza kuondoa migogoro itakayojitokeza,” alisema Kiswaga.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Taifa wa TAPSEA, Leah Mwamba, aliwashukuru wanachama kwa kumpa dhamana ya kuwaongoza na kuahidi kushirikiana nao katika kuhakikisha chama kinafikia malengo yake. Amesema tukio la uapisho ni hatua muhimu katika safari ya uongozi na kuomba wanachama waendelee kuwaunga mkono.
“Ninatoa shukrani zangu za pekee kwa wote walioungana nasi katika historia hii. Jambo hili la uapisho ni kubwa sana, hivyo tunaomba mzidi kutuombea tufanye vyema katika uongozi,” alisema Mwamba.
Naye Katibu Mkuu wa TAPSEA, Hellen Magati, aliwashukuru wageni na wadau waliohudhuria hafla hiyo, akiahidi kuwa uongozi mpya utashirikiana na wanachama na wadau mbalimbali katika kutekeleza majukumu yake na kuimarisha chama.
Viongozi wengine walioapishwa ni pamoja na Makamu Mwenyekiti, Zainab Ibrahim Ally, Naibu Katibu Mkuu, Halima Twaha Mgulo, Mweka Hazina, Nyanza Msongela, pamoja na wajumbe wengine waliochaguliwa katika uongozi huo.

Na Janeth Raphael - MichuziTv - Bungeni Dodoma
Serikali imesema haina mamlaka ya kuzipangia benki za biashara viwango vya riba za mikopo, kwa kuwa gharama hizo huamuliwa na mwenendo wa soko pamoja na sababu mbalimbali za kiuchumi na kiutendaji.
Kauli hiyo imetolewa leo, Agosti 26, 2026, na Naibu Waziri wa Fedha, Laurent Luswetula, wakati akijibu swali la Mbunge wa Mpanda Mjini, Haidary Sumry, Bungeni kuhusu hatua zinazochukuliwa na Serikali kupunguza riba za mikopo ya biashara ili kuwawezesha wafanyabiashara kulipa madeni yao kwa wakati.
Luswetula amesema Serikali haiingilii moja kwa moja upangaji wa riba katika benki za biashara, kwa sababu viwango hivyo huwekwa kwa kuzingatia misingi ya soko.
Ameeleza kuwa miongoni mwa mambo yanayochangia kuamua kiwango cha riba ni mfumuko wa bei, hatari ya mkopaji kushindwa kurejesha mkopo, gharama za uendeshaji wa benki pamoja na kiwango cha faida kinacholengwa na taasisi husika ya fedha.
Hata hivyo, amesema Serikali inaendelea kuchukua hatua za kisera na kiusimamizi zinazolenga kupunguza gharama za mikopo na kuongeza fursa kwa wananchi na wafanyabiashara kupata huduma za fedha kwa masharti nafuu.
Kwa mujibu wa Naibu Waziri, Serikali inaendelea kutekeleza sera za fedha zinazolenga kudhibiti mfumuko wa bei, ambao ni miongoni mwa vigezo vinavyozingatiwa katika upangaji wa viwango vya riba.
Amesema Benki Kuu ya Tanzania (BoT) imekuwa ikirekebisha kiwango cha Riba ya Benki Kuu (CBR) kulingana na mwenendo wa uchumi, hatua inayolenga kudhibiti mfumuko wa bei na kuhakikisha kunakuwa na ukwasi wa kutosha katika uchumi.
Luswetula pia ametaja kuanzishwa kwa Price Comparator System, mfumo unaolenga kuongeza uwazi katika sekta ya fedha kwa kuwawezesha wananchi kulinganisha viwango vya riba na gharama nyingine za mikopo zinazotozwa na taasisi mbalimbali za kifedha.
Amesema mfumo huo unatarajiwa kuongeza ushindani miongoni mwa benki na taasisi za fedha, jambo ambalo linaweza kuchangia kupunguza gharama za mikopo na kuwasaidia wakopaji kufanya maamuzi sahihi kabla ya kukopa.
Aidha, Serikali imeendelea kuhimiza matumizi ya Credit Reference Bureau, mfumo unaohifadhi taarifa kuhusu historia ya ukopaji na ulipaji wa madeni ya wateja.
Naibu Waziri amesema matumizi ya taarifa hizo yanawezesha benki kutathmini kwa usahihi uwezo na historia ya mkopaji, hivyo kupunguza vihatarishi vya mikopo kutolipwa na gharama zinazotumika katika tathmini ya wakopaji.
Amesema hatua hizo, kwa pamoja, zinaweza kusaidia kupunguza gharama za mikopo kwa wananchi na wafanyabiashara, licha ya Serikali kutokuwa na mamlaka ya kuweka moja kwa moja viwango vya riba vinavyotozwa na benki za biashara.
Kwa hiyo, Serikali imeeleza kuwa mkakati wake ni kutumia sera za fedha, kuongeza ushindani na uwazi katika sekta ya kifedha pamoja na kuimarisha mifumo ya taarifa za wakopaji, ili kuchochea upatikanaji wa mikopo yenye gharama nafuu zaidi.
Tume ya Madini imewapa siku 30 wamiliki wa baadhi ya miradi ya msaada wa kiufundi kurekebisha mapungufu yaliyobainika katika utekelezaji wa shughuli zao, huku ikionya kuwa kushindwa kutekeleza matakwa hayo ndani ya muda uliowekwa kunaweza kusababisha kuchukuliwa kwa hatua za kisheria, ikiwemo kufutwa kwa hati au idhini za msaada wa kiufundi.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma Katibu Mtendaji, Tume ya Madini Mhandisi Ramadhani Lwamo amesema hatua hiyo imekuja baada ya Tume kufanya ukaguzi wa miradi ya msaada wa kiufundi na kubaini kuwa baadhi yake haitekelezwi kwa kuzingatia matakwa ya sheria, kanuni na masharti yanayosimamia sekta ya madini nchini.
Kwa mujibu wa matokeo ya ukaguzi huo, jumla ya miradi 42 imebainika kuwa haifanyi kazi, wakati miradi mingine 86 inaendelea na shughuli zake lakini imeonekana kuwa na changamoto na mapungufu mbalimbali yanayohitaji kurekebishwa.
Kutokana na hali hiyo, Tume ya Madini imewapatia wamiliki wa miradi husika hati za makosa, zikiwaelekeza kurekebisha mapungufu yaliyoainishwa na kuwasilisha mrejesho ndani ya siku 30 tangu kutolewa kwa maelekezo hayo.
Tume imesisitiza kuwa muda huo si wa kupuuzwa, kwani iwapo wamiliki wa miradi watashindwa kutekeleza matakwa yaliyowekwa, hatua zaidi za kisheria zitachukuliwa kwa mujibu wa sheria. Miongoni mwa hatua zinazoweza kuchukuliwa ni kufutwa kwa hati au idhini zinazohusiana na shughuli za msaada wa kiufundi.
Aidha, Tume imewataka wanufaika wa huduma za msaada wa kiufundi kuhakikisha shughuli zao zinafanyika kwa kuzingatia kikamilifu sheria, kanuni na masharti ya sekta ya madini, badala ya kusubiri hatua za utekelezaji zichukuliwe.
Katika maelekezo yake, Tume imekazia umuhimu wa kuzingatia masuala ya utunzaji na uhifadhi wa mazingira, usalama na afya mahali pa kazi, pamoja na kuhakikisha shughuli zote za uchimbaji na huduma za kiufundi zinafanyika kwa mujibu wa masharti yaliyowekwa na mamlaka husika.
Tume imeeleza kuwa utekelezaji wa masharti hayo ni muhimu katika kuhakikisha shughuli za madini zinafanyika kwa usalama, zinazingatia mazingira na zinatoa manufaa yanayokusudiwa kwa wachimbaji, jamii zinazozunguka maeneo ya miradi na Taifa kwa ujumla.
Aidha, Tume imeonya kuwa itaendelea kufanya ukaguzi wa mara kwa mara katika miradi ya msaada wa kiufundi ili kubaini changamoto, kuhakikisha wamiliki wanazingatia matakwa ya kisheria na kuchukua hatua stahiki pale ambapo kutakuwa na ukiukwaji.
Hatua hiyo inalenga kuimarisha usimamizi wa shughuli za madini na kuhakikisha kuwa miradi yenye idhini inatekelezwa kwa ufanisi, kwa kuzingatia sheria na viwango vinavyotakiwa, huku ikihakikisha kuwa rasilimali za madini zinatumika kwa manufaa ya uchumi, jamii na Taifa.
Kwa wamiliki wa miradi iliyobainika kuwa na mapungufu, siku 30 zilizotolewa na Tume sasa ni muda wa kuchukua hatua za haraka kurekebisha kasoro hizo na kuwasilisha mrejesho, vinginevyo wanaweza kukabiliwa na hatua kali zaidi za kisheria, ikiwemo kupoteza hati au idhini zao.
Serikali imesema haina mpango wa kuunda Tume maalum ya Taifa ya kutatua migogoro ya ardhi nchini, badala yake imeandaa Mkakati wa Kudumu wa Utatuzi wa Migogoro ya Ardhi Nchini utakaotumika na taasisi mbalimbali za Serikali katika kushughulikia migogoro hiyo.
Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Kaspare Mmuya, wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Asha Ramadhani Baraka, aliyetaka kujua lini Serikali itaunda Tume itakayokuwa na jukumu la kutatua migogoro ya ardhi katika maeneo mbalimbali nchini.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri Mmuya amesema Serikali imeona umuhimu wa kutumia mfumo wa pamoja unaowezesha taasisi zinazohusika kushughulikia migogoro ya ardhi kwa utaratibu unaofanana, badala ya kuanzisha Tume nyingine.
Amesema Mkakati huo utaiwezesha Serikali kuwa na kanzidata moja inayohifadhi taarifa za migogoro ya ardhi nchini, hatua itakayosaidia kuondoa changamoto ya mgogoro mmoja kushughulikiwa na taasisi zaidi ya moja na hatimaye kutolewa kwa maamuzi yanayotofautiana.
Kwa mujibu wa Naibu Waziri, mfumo huo utasaidia kuongeza uelewa, uwazi na uwajibikaji miongoni mwa taasisi zinazohusika, huku ukiongeza kasi ya kushughulikia na kutatua migogoro ya ardhi.
Amesema Serikali inalenga kupitia mkakati huo kuimarisha amani, umoja na mshikamano katika jamii, sambamba na kuboresha mazingira ya uwekezaji katika ardhi na kuchochea ukuaji wa uchumi wa nchi.
Naibu Waziri Mmuya amesema kwa sasa Mkakati wa Kudumu wa Utatuzi wa Migogoro ya Ardhi Nchini upo katika hatua za ukamilishaji na mara utakapokamilika utaanza kutumiwa na taasisi zote husika.
Hatua hiyo inatarajiwa kuweka mfumo mmoja wa kitaifa wa kushughulikia migogoro ya ardhi, kwa kuimarisha uratibu wa taasisi za Serikali na kuhakikisha migogoro inashughulikiwa kwa ufanisi, uwazi na kwa maamuzi yanayokwenda sambamba.
Zaidi ya Shilingi milioni 700 zinatarajiwa kutumika katika ujenzi wa Shule ya Sekondari ya Kashishi iliyopo Kata ya Nyakamwaga Halmashauri ya Wilaya ya Geita. Shule hiyo inatarajiwa kuondoa adha ya wanafunzi kutembea umbali mrefu kufuata shule.
Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026, Ndugu Wazo Michael Mwang’onda, ndiye aliyeweka jiwe la msingi katika ujenzi wa shule hiyo wakati Mwenge ulipofika Halmashauri ya Wilaya ya Geita.
Akizungumza baada ya kuweka jiwe la msingi, Mwang’onda amesema ameridhishwa na mradi huo ambao mpaka sasa umefikia asilimia 75 ya utekelezaji. Amesema ni shule ya kwanza ya Serikali yenye muonekano wa gorofa katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita.
Ameeleza kuwa shule hiyo ilianzishwa kwa nguvu za wananchi na baadaye kuungwa mkono na mdau wa maendeleo, Mhe. Evarist Gervas, ambaye ametumia zaidi ya Shilingi milioni 300 kukamilisha miundombinu.
Mwang’onda amesema mradi huo utakuwa na madarasa zaidi ya 8, matundu 12 ya vyoo pamoja na ofisi mbalimbali. Pia ametoa wito kwa wadau wengine kuiga mfano wa Mhe. Gervas kwa kuunga mkono juhudi za wananchi katika kukuza maendeleo ya elimu Kata ya Nyakamwaga.
Kwa upande wao wananchi wa Kijiji cha Kashishi wamesema walianzisha ujenzi wa shule hiyo ili kupunguza umbali wa watoto kwenda kusoma. Wamesema hapo awali wanafunzi walikuwa wakitembea umbali mrefu hadi Shule ya Sekondari Nyakamwaga na wengi waliishia kukatisha masomo.













.jpeg)


.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)