Na Karama Kenyunko, Michuzi TV
KATIKA ghala moja la kuhifadhi mazao nchini Tanzania, mfumo wa kielektroniki unapiga kengele. Dakika chache baadaye, ujumbe unaingia kwenye simu ya msimamizi wa ghala ukionya kuwa kiwango cha joto na unyevunyevu kimeanza kufikia mazingira yanayoweza kuzalisha sumu kuvu kwenye mahindi yaliyohifadhiwa.

Onyo hilo halihusu moto wala uvamizi wa wahalifu. Linaashiria uwepo wa mazingira yanayoweza kuchochea kuzalishwa kwa sumu kuvu kwenye mazao ya chakula.

Ingawa mazao kama mahindi, mtama na karanga ni sehemu ya chakula cha kila siku kwa mamilioni ya Watanzania, si wananchi wote wanaofahamu kuwa yanaweza kuwa chanzo cha hatari kubwa kiafya yanapoathiriwa na sumu kuvu.

Unapuzungumzia sumu kuvu katika mazao kama vile mtama, mahindi, na karanga, siyo Wananchi wote wanafamu kuwa sumu kuvu inaweza kuleta madhara kwa binadamu na mifugo na hatimaye kusababisha kansa ya ini.

Sumu kuvu ni aina ya sumu inayotengenezwa na kuvu au fangasi wanaoota kwenye mazao mbalimbali hasa nafaka kama vile mahindi, mtama, ngano, mchele na ulezi. Kuvu hao wanapoota huonekana kama ukungu. Mahindi ndiyo nafaka inayoshambuliwa zaidi na uchafuzi wa sumu kuvu ikilinganishwa na nafaka nyingine.

Mazao mengine yanayoweza kushambuliwa na fangasi hawa ni pamoja na mbegu za mafuta kama karanga, pamba, alizeti na korosho; mihogo mikavu; viungo vya chakula mfano iliki na mdalasini; mboga za majani pamoja na matunda yaliyokaushwa.

Kwa mujibu wa Shirika la Chakula Duniani (FAO), sumu kuvu huharibu karibu asilimia 25 au zaidi ya chakula kinachozalishwa duniani kila mwaka.

Kutokana na madhara hayo, Idara ya Teknolojia na Sayansi ya Vyakula, Ndaki ya Kilimo ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, imetengeneza teknolojia mpya ya mfumo wa kidigitali wa kudhibiti vigezo vinavyosababisha uzalishaji wa sumu kuvu (aflatoxins) ili kugundua viatarishi vinavyosababisha sumu kuvu katika mazao.

Hii si teknolojia kutoka nje ya nchi. Ni ubunifu uliotengenezwa Tanzania na timu ya watafiti wakiongozwa na Profesa Mshiriki Lilian Kaale kutoka Idara ya Teknolojia na Sayansi ya Vyakula, Ndaki ya Kilimo Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Profesa Kaale ambaye pia ni Mkurugenzi wa Ubunifu na Ujasiriamali chuoni hapo anasema ubunifu huo unalenga kudhibiti sumu kuvu kabla haijazalishwa kwenye mazao yaliyohifadhiwa maghalani.

Anaeleza kwamba safari ya utafiti huo ilianza mwaka 2018 baada ya kupata ufadhili wa takribani Sh milioni 100 kutoka UNESCO.

“Niliona tatizo la sumu kuvu ni kubwa sana Tanzania. Mbali na kuharibu mazao, mazao yaliyoingiliwa na sumu hii yanaathiri afya za binadamu kwa kiwango kikubwa hususan kuchangia saratani ya ini,” anasema.

Baadaye aliomba ufadhili kutoka Tume ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) ambapo alipata shilingi milioni 120 ili kuendeleza tafiti zaidi kuhusu namna ya kutumia teknolojia ya kidigitali kugundua na kuzuia mazingira yanayochochea uzalishaji wa sumu kuvu.

Kwa mujibu wa Kaale, sumu hiyo huzalishwa na fangasi aina ya aspergillus pale mazingira fulani yanapokuwepo, hasa joto na unyevunyevu mkubwa.

“Vimelea hivi vinaweza kuwepo kwenye mazao lakini visizalishe sumu kuvu mpaka mazingira yanayowawezesha kufanya hivyo yatokee,” anasema.

Anataja mahindi, karanga na mtama kuwa miongoni mwa mazao yanayoathirika zaidi.

Anasema ubunifu huo umetengenezwa kwa kutumia vifaa vinavyopima kiwango cha unyevunyevu, joto na hali ya hewa ndani ya ghala.

Mfumo huo unapogundua mazingira yanaanza kufikia kiwango hatarishi cha kuzalisha sumu kuvu, kengele huanza kulia na ujumbe hutumwa moja kwa moja kwa msimamizi wa ghala kupitia simu.

“Ukidhibiti mazingira hayo mapema, fangasi hawawezi kuzalisha sumu kuvu,” anasema Profesa Kaale.

Anaeleza kwamba mfumo huo umeunganishwa na simu za wasimamizi wa maghala kuwawezesha kuwasha feni au kufungua milango ili kupunguza joto na unyevunyevu kabla hali haijafikia kiwango hatari.
Kwa mujibu wake, mazao baada ya kuvunwa hubaki hai na huendelea kuzalisha joto na unyevunyevu, hali hiyo huongeza uwezekano wa kuzalishwa kwa sumu kuvu wakati wa uhifadhi.

“Tafiti zinaonesha upotevu mkubwa wa mazao hutokea baada ya kuvuna, hasa kipindi cha uhifadhi,” anasema.

Anafafanua kuwa kwa sasa teknolojia hiyo imefungwa katika ghala lililopo Chemba mkoani Dodoma chini ya usimamizi wa Wizara ya Kilimo na wadau wengine wa serikali kama mfano wa majaribio tangu Agosti mwaka jana.

Kwa sababu ya gharama zake, Profesa Kaale anasema mkulima mmoja mmoja hawezi kuimudu kwa sasa na kwamba inalenga zaidi maghala makubwa ya serikali na wafanyabiashara wakubwa.

"Tumeshirikiana na serikali kwa sababu athari za sumu kuvu ni za taifa. Mfanyabiashara binafsi anaweza kupata mfumo huo kwa gharama ya takribani Sh milioni 30 ili kuusimika kwenye ghala lake," anasema.

Kwa mujibu wa Profesa Kaale, sumu kuvu ina madhara makubwa kwa ini na imehusishwa pia na magonjwa yasiyoambukiza pamoja na udumavu kwa watoto.

Anasema tatizo hilo linaweza kuathiri mamilioni ya Watanzania kwa sababu zaidi ya watu milioni 50 hutumia mahindi na karanga kama chakula cha kila siku.

“Ukilisha wanyama pumba zenye sumu kuvu, madhara yanaweza kurudi kwa binadamu kupitia mnyororo wa chakula,” anasema.

Anakumbusha tukio la mwaka 2015 mkoani Dodoma ambapo watu walifariki baada ya kula chakula kilichoathiriwa na sumu kuvu.

Kwa upande wake, Ibrahim Kinyoro ambaye ni mwanafunzi wa PhD anayesimamiwa na Profesa Kaale, anasema anakubaliana na teknolojia hiyo kwa kiasi kikubwa katika kukabiliana na sumu kuvu nchini.

Anasema teknolojia mbalimbali zimetumiwa na mtafiti huyo ikiwemo mifumo ya kengele "alarm" ya kutambua uwepo wa sumu kuvu.

"Teknolojia nzuri na nyingi zipo tayari na zimetoa matokeo isipokuwa uwekezaji na uendelevu wa teknolojia hizo kutumiwa na wakulima una gharama kubwa," anaeleza.

Kinyolo anasema ni wakati wa serikali, watunga sera na sekta binafsi kushirikiana kuwekeza katika teknolojia na kuwakomboa wakulima kukabiliana na sumu kuvu.

Anaeleza kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa na namna wanavyozalisha mazao yao, kuvu wataendelea kukua.

Kinyoro anasema sumu kuvu ikishaingia kwenye mahindi au karanga kuna baadhi ya hatua zikifanywa hupunguza kwa asilimia kidogo uwepo wake ikiwemo kuyachagua moja moja, kupepeta au kukoboa.

"Hizi ni njia za asili zinazotumika kuondoa sumu kuvu lakini mazao haya yakishambuliwa kwa wingi, zile unazozitoa kwa macho ndiyo ambazo zimeshambuliwa kwa kiwango kikubwa na zipo nyingine huwezi kuziona kwa macho."

Kwa upande wake, Mshauri wa Sera wa taasisi ya GRAIN, Leticia William, anasema sumu kuvu ni hatari sana ikiingia mwilini mwa binadamu au mnyama kwani inaua kimyakimya na inaweza kusababisha saratani.

Anasema ongezeko la uchafuzi wa sumu kuvu kwenye mazao ya chakula na chakula cha mifugo linaendelea kuwa tishio kubwa kwa afya ya binadamu na wanyama nchini Tanzania.

“Kutokana na hali hiyo, watu, watoto, ng’ombe, kuku, nguruwe na wanyama wengine wako kwenye hatari kubwa kutokana na matumizi ya mazao yaliyoathirika,” anasema.

Naye Mchumi Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Dkt. Deogratius Lwezaura, anasema utafiti uliofanywa kati ya mwaka 2012 na 2014 katika kanda saba za kilimo ulithibitisha kuwa sumu kuvu inaweza kusababisha saratani ya ini, mzio, kudumaa kwa watoto pamoja na kuathiri ukuaji wa akili.

Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na Profesa Martin Kimanya kwa kushirikiana na watafiti wa Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela mwaka 2016, Tanzania ilipoteza zaidi ya Sh bilioni 550 kila mwaka kutokana na athari za kiafya na kiuchumi zinazosababishwa na sumu kuvu kwenye mazao ya chakula.

Hasara hiyo inajumuisha mazao yanayokataliwa katika masoko ya ndani na nje pamoja na gharama za matibabu ya magonjwa kama saratani ya ini.

Ripoti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) pia ilieleza kuwa bara la Afrika hupoteza wastani wa Dola za Marekani milioni 670 kila mwaka kutokana na bidhaa za kilimo kukataliwa katika masoko ya nje kwa sababu ya uchafuzi wa sumu kuvu.

Katika taifa linalotegemea kilimo, vita dhidi ya sumu kuvu si suala la maabara pekee. Ni suala la afya, usalama wa chakula na mustakabali wa uchumi wa taifa.

-Ni dawa zilizokamatwa ndani ya jahazi la Al Arab lililokuwa na raia saba wa Iran Bahari ya Hind

Na Mwandishi Wetu

MAMLAKA ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imeteketeza kilogramu 504.36 za dawa za kulevya aina ya heroin katika kiwanda cha saruji cha Dangote kilichopo mkoani Mtwara.

Taarifa iliyotolewa na Mamlaka hiyo kwa vyombo vya habari imeeleza kuwa uteketezaji huo umefanyika kutokana na amri ya Mahakama Kuu Masijala Ndogo ya Mtwara baada ya kukamilika kwa hatua za kisheria dhidi ya watuhumiwa waliohusika na dawa hizo.

Dawa hizo zilikamatwa ndani ya jahazi la Al Arab lililokuwa na raia saba wa Iran katika Bahari ya Hindi ndani ya eneo la kiuchumi la Tanzania.

Uteketezaji huo umefanyika kwa mujibu wa Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Sura ya 95 inayoruhusu kuteketezwa kwa vielelezo vya dawa za kulevya baada ya taratibu za kisheria kukamilika au wakati shauri linaendelea kwa idhini ya mahakama.

Katika hatua nyingine Mamlaka imeendelea kusisitiza umuhimu wa kuimarisha huduma za tiba na utengemao kwa watu wenye uraibu wa dawa za kulevya hususan katika ukanda wa kusini mwa Tanzania.

Katika kutekeleza azma hiyo, DCEA itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuwezesha upatikanaji wa huduma za MAT pamoja na kuanzishwa kwa nyumba za upataji nafuu (sober houses) ili kusaidia waraibu kupata huduma stahiki na kurejea katika maisha yenye tija kwa jamii.

Aidha imesema itaendelea kushirikiana na vyombo vya dola, wadau mbalimbali pamoja na wananchi katika kuzuia usafirishaji, biashara na matumizi ya dawa za kulevya nchini.

“Mamlaka itaendelea kuimarisha utoaji wa elimu kwa umma kuhusu madhara ya dawa za kulevya na umuhimu wa ushiriki wa jamii katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya.”






▪️Aonya dhidi ya vitendo vya uchochezi, kujiteka na propaganda zinazolenga kuwagombanisha Watanzania

▪️Asema Serikali imejikita kusikiliza wananchi na kutatua kero zao badala ya mijadala ya uchaguzi

▪️Awataka wananchi kuendelea kulinda mshikamano na utulivu wa Taifa


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amevitaka vyombo vya ulinzi na usalama kuendelea kuwa macho dhidi ya vitendo vinavyolenga kuvuruga amani ya nchi huku akisisitiza kuwa Serikali itaendelea kusimamia usalama wa wananchi na mali zao.

“Kuweni macho na njama za aina hii, shughulikeni na waovu wa aina hii. Mliweza lile la Kibiti, mliweza lile la Amboni na mambo mengine mengi mmeweza. Kuweni macho kuhakikisha michezo ya aina hiyo haifanikiwi huku mkihakikisha usalama wa raia wetu na mali zao unaendelea kulindwa,” amesema Dkt. Mwigulu.

Dkt. Mwigulu amesema hayo leo Jumamosi, Mei 23, 2026 alipozungumza na wananchi wa Manispaa ya Iringa katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika viwanja vya Kichangani mkoani Iringa.

Amesema amani ni msingi wa maendeleo ya Taifa na kwamba Watanzania wanapaswa kuendelea kulinda mshikamano wa kitaifa na kukataa vitendo vya uchochezi vinavyoweza kusababisha migawanyiko ya kisiasa, kidini au kijamii.

“Amani ni msingi wa maendeleo ya taifa letu. Kila mwananchi ana wajibu wa kuhakikisha nchi yetu inaendelea kuwa salama na yenye mshikamano,” amesema.

Aidha, Waziri Mkuu amesema zipo njama mbalimbali zinazolenga kuwagombanisha Watanzania kupitia siasa, dini na taarifa za upotoshaji huku akiwataka wananchi kuwa makini na watu wanaowachochea kufanya vitendo vinavyohatarisha usalama wa nchi.

“Tupuuze na wala tusiwe na ushirika na mtu anayekutuma kuvunja amani wakati yeye hayupo hapo na anajua yeye hataathirika,” amesema.

Kadhalika, Dkt. Mwigulu amesema baadhi ya matukio yanayoendelea kujitokeza nchini yakiwemo madai ya watu kujiteka au kushambuliwa yanapaswa kutazamwa kwa umakini mkubwa kwa kuwa baadhi yake yanaweza kuwa sehemu ya njama za kuwagawa Watanzania na kuichonganisha Serikali na wananchi wake.

“Hizi ni ajenda maalum. Hii ni michezo ambayo inalenga kutengeneza hasira na kuwafanya watu wachukiane,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Serikali imejikita zaidi katika kutatua changamoto za wananchi na kusukuma maendeleo badala ya kuendelea kujadili siasa za uchaguzi muda mfupi baada ya uchaguzi mkuu kumalizika.

“Taifa linapotakiwa kupiga hatua, tujadili namna ya kutatua kero za wananchi badala ya kutumia muda mwingi kujadili uchaguzi,” amesema.

Amesema yeye binafsi ameendelea kufanya ziara mbalimbali za kusikiliza wananchi, kupokea changamoto zao na kuhakikisha Serikali inazitatua kwa wakati ili wananchi waendelee na shughuli zao za maendeleo.

“Watu wanahitaji kusikilizwa, wanahitaji kutatuliwa changamoto zao na wanahitaji maendeleo. Hiyo ndiyo kazi ambayo Serikali imepewa na wananchi,” amesema.

Aidha, Dkt. Mwigulu amesema Tanzania imeendelea kuwa mfano wa mshikamano na uvumilivu wa kidini na kijamii barani Afrika kutokana na misingi iliyoasisiwa na viongozi waasisi wa Taifa.

“Hii ndiyo nchi ambayo Mungu ametupatia na Baba wa Taifa ameturithisha. Tukatae vibaraka wanaotaka kuligawa Taifa letu,” amesema.

Waziri Mkuu pia amewaomba viongozi wa dini, wazee wa mila, viongozi wa kisiasa na wananchi kwa ujumla kuendelea kuhubiri amani, mshikamano na uzalendo ili taifa liendelee kuwa salama na lenye umoja.










▪️Asema mradi huo utafungua fursa mpya za uchumi na kupunguza msongamano wa magari mjini Iringa

▪️Aagiza wakandarasi kuwalipa kwa wakati wadaiwa wao

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuwekeza katika miradi ya kimkakati ya miundombinu ili kuboresha usafiri, kuongeza ufanisi wa uchukuzi na kufungua fursa mpya za maendeleo ya kiuchumi nchini.

“Barabara hii ni muhimu kwa uchumi wa Mkoa wa Iringa na Taifa kwa ujumla. Itasaidia kupunguza msongamano wa magari, kuongeza biashara na kuchochea ukuaji wa mji wa Iringa,” amesema Dkt. Nchemba.

Amesema hayo leo Jumamosi, Mei 23, 2026 wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa Barabara ya Mchepuo ya Mji wa Iringa (Iringa Municipal Bypass) yenye urefu wa kilomita 7.3 inayojengwa kwa kiwango cha lami mkoani Iringa.

Mradi huo unaotekelezwa na kampuni ya SINOHYDRO Corporation Limited kwa usimamizi wa TANROADS kupitia kitengo chake cha TECU, unagharimu shilingi bilioni 41.6.

Akizungumza baada ya kupokea taarifa ya utekelezaji wa mradi huo, Waziri Mkuu amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kutekeleza miradi mikubwa ya barabara nchini kwa lengo la kuimarisha uchumi na kurahisisha huduma za usafiri na uchukuzi.

Amesema barabara hiyo itakuwa suluhisho la kudumu la msongamano wa magari katika mji wa Iringa hususan katika eneo la mlima wa Ipogoro ambalo limekuwa likikumbwa na ajali na changamoto za usafiri kutokana na ongezeko kubwa la idadi ya watu, magari na vyombo vingine vya usafiri.

“Ndugu zangu wana Iringa, Mheshimiwa Rais amejipambanua kuwa ni Rais wa matokeo. Akisema jambo analitekeleza, na ndiyo maana mnaendelea kuona miradi mikubwa ya barabara ikitekelezwa karibu kila kona ya nchi,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amewataka wakandarasi wanaotekeleza miradi ya Serikali kuhakikisha wanawalipa kwa wakati wakandarasi wadogo, mafundi na vibarua wanaoshiriki katika utekelezaji wa miradi hiyo.

“Kadri wanavyopata fedha, wawalipe wale wanaotekeleza mradi pamoja nao. Sio vizuri mradi ukamilike wakati wengine waliotoa huduma wanadai malipo yao,” amesema.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Ujenzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya amesema mradi huo ni sehemu ya utekelezaji wa mkakati wa Serikali wa kujenga barabara za mchepuo katika miji mikubwa ili kupunguza msongamano wa magari na kuongeza ufanisi wa usafiri wa mizigo nchini.

Amesema Serikali pia inaendelea kutekeleza miradi mingine ya barabara za mchepuo katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo Dodoma, Mbeya, Morogoro, Mwanza, Arusha na Tanga.

Awali akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa mradi huo, Kaimu Meneja wa TANROADS Mkoa wa Iringa, Mhandisi Hosea Machaka amesema utekelezaji wa mradi umefikia asilimia 38.5 huku kazi mbalimbali zikiendelea ikiwemo ulipuaji wa miamba, ujazaji wa kifusi, ujenzi wa makalavati pamoja na ujenzi wa njia za mchepuo.

Amesema wananchi 186 walioathiriwa na mradi huo wamelipwa fidia yote yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 4.6, hatua iliyosaidia kuondoa changamoto za upatikanaji wa eneo la mradi.

Naye Mbunge wa Iringa Mjini, Fadhili Ngajilo amesema wananchi wa Iringa wameupokea mradi huo kwa matumaini makubwa kutokana na mchango wake katika kuboresha usafiri na kuchochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi katika mji huo.











Mkoa wa Ruvuma umeendelea kujizolea umaarufu katika sekta ya madini baada ya makaa ya mawe yanayochimbwa katika wilaya za Mbinga, Songea na Nyasa kufungua masoko katika nchi mbalimbali za Afrika na Asia, huku zaidi ya tani milioni 3.6 zikizalishwa mwaka 2024/2025 na kuchochea ajira, biashara na matumizi ya nishati safi.

Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Ruvuma, Mhandisi Alphonce Bikulamchi amesema shughuli za utafiti, uchimbaji na uchakataji wa makaa ya mawe zinazofanywa na makampuni pamoja na wadau mbalimbali zimekuwa na mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa Mkoa wa Ruvuma na Taifa kwa ujumla.

Amesema makaa hayo yenye ubora wa hali ya juu yanatumika katika viwanda vya saruji, usafishaji wa vyuma na shughuli nyingine za viwandani, huku sehemu ya uzalishaji ikipelekwa katika masoko ya Kenya, Uganda, Rwanda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).

“Migodi ya makaa ya mawe ya Ruvuma imeendelea kuvutia wawekezaji kutokana na ubora wa madini hayo, hali iliyosaidia kufungua masoko mapya katika baadhi ya nchi za Asia na Ulaya,” amesema Mhandisi Bikulamchi.

Ameeleza kuwa ukuaji wa sekta hiyo umechangiwa na kuongezeka kwa uwekezaji pamoja na mahitaji ya nishati duniani tangu mwaka 2019/2020, jambo lililoongeza mchango wa sekta ya madini katika mapato ya Serikali na maendeleo ya Mkoa wa Ruvuma.

Katika hatua nyingine, wadau wa makaa ya mawe mkoani humo wameendelea kuunga mkono agenda ya matumizi ya nishati safi kupitia uzalishaji wa mkaa mbadala unaotokana na makaa ya mawe, wakiwemo Mgodi wa Jitegemee uliopo Wilaya ya Mbinga na Kampuni ya Suzlon ya Wilaya ya Songea.

Migodi hiyo imeendelea kuzalisha mkaa wa nishati safi unaotajwa kusaidia kupunguza matumizi ya mkaa wa kawaida unaotokana na ukataji miti, hatua inayochangia uhifadhi wa mazingira na kupunguza uharibifu wa misitu.

Msimamizi wa Mauzo na Uendeshaji wa Mgodi wa Jitegemee, Mark Tarimo amesema kampuni hiyo imetoa zaidi ya ajira 500 kupitia nafasi za kudumu na mikataba ya mwaka mmoja, huku bidhaa zake zikisafirishwa katika nchi za Afrika Mashariki na Falme za Kiarabu (UAE).

Tarimo amesema kampuni hiyo pia imetekeleza miradi mbalimbali ya kijamii ikiwemo ujenzi wa shule katika Kijiji cha Ruanda, zahanati katika Kijiji cha Luhagara pamoja na usambazaji wa majiko ya nishati safi kwa wananchi.

Naye Mkurugenzi wa Mgodi wa Suzlon, Jigar Chandarana amesema mkaa wa nishati safi unaozalishwa na kampuni hiyo ni mbadala wa mkaa wa kawaida kwa kuwa hudumu kwa muda mrefu, ni nafuu kwa matumizi ya nyumbani na husaidia kulinda mazingira dhidi ya uharibifu wa misitu.

Aidha, Mhandisi Bikulamchi amewataka wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kutumia fursa zilizopo katika sekta ya madini mkoani Ruvuma, huku akiwahimiza vijana kushiriki katika shughuli za uchimbaji, usafirishaji na utoaji wa huduma zinazohusiana na sekta hiyo.









Na. Vero Ignatus. 

Mwanadiplomasia na Mratibu wa Makongamano ya Vijana, Ndugu Omary Abdul Punzi, amewashauri vijana nchini kuacha kufuata mikumbo isiyo na tija na badala yake waithamini nchi yao kwa kutanguliza uzalendo mbele. 

Akizungumza katika mahojiano maalum na Michuzi Blog, Punzi amesisitiza kuwa amani ya nchi haitofautiani na utulivu wa kisiasa, bali inategemea kwa kiasi kikubwa jinsi vijana wanavyoheshimu utamaduni wao na kushirikiana kikamilifu na mihimili nane muhimu inayolinda na kulea taifa. 

Amewasihi vijana kuwa makini na ushawishi hasi wa utandawazi na makundi yasiyo na maadili yanayotishia mustakabali wa nchi.

Akionyesha masikitiko yake, Punzi amekumbusha kuwa Tanzania ni urithi wa thamani tulioachiwa na waasisi wetu, hivyo hakuna nchi nyingine mbadala ikiwa vijana wataharibu hii iliyopo. 

Alibainisha kuwa miongozo na desturi nzuri zilizowekwa na wazee wa kimila tangu zamani hazikuwa za kizamani, bali zililenga kulinda utu na heshima ya jamii. 

Alionya kuwa sasa vijana wanatupa dhahabu yao kwa sababu tu inaonekana ya kienyeji na kuokota shaba ya kigeni kwa kuwa inang’aa, jambo linalohitaji mabadiliko ili mila na desturi zilizokubalika zisafishwe na kuendelezwa badala ya kufutwa kabisa.

Katika uchambuzi wake, Punzi alifafanua jinsi mihimili nane ya amani na malezi inavyopaswa kuwa dira kwa kijana mzalendo. Mhimili wa kwanza ni shule ambayo ndiyo msingi wa maarifa, nidhamu na malezi ya awali ya kiakili yanayomfanya kijana kuwa raia mwema. 

Hii inaenda sambamba na Jeshi la Polisi ambalo ni chombo cha usalama wa raia na mali zao kinachotegemea ushirikiano wa karibu na vijana kupitia ulinzi shirikishi. Vivyo hivyo, Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) linatajwa kama jukwaa la kuwajenga vijana katika ukakamavu na uzalendo, huku Jeshi la Ulinzi la Wananchi Tanzania (JWTZ) likiwa ngome kuu ya ulinzi wa mipaka ya nchi na alama ya mamlaka ya taifa.

Mihimili mingine inayokamilisha ngome hii ya malezi na ulinzi inajumuisha Idara ya Usalama wa Taifa, chama cha Skauti, taasisi za kidini, pamoja na mila na desturi nzuri ambazo ndizo msingi wa utambulisho wa Mwafrika unaosisitiza heshima, mshikamano na utatuzi wa migogoro kwa njia ya mazungumzo badala ya vurugu. 

Punzi amewataka vijana kutokubali kuwa bendera inayofuata upepo wa mambo yanayoonekana maarufu kwenye mitandao ya kigeni, kwani kufanya hivyo ni kupoteza dira. Alizitaka taasisi zote za elimu, dini na vikosi vya usalama kushirikiana kwa karibu ili kuwatengenezea vijana mazingira wezeshi yatakayowafanya kuwa walinzi namba moja wa amani na maendeleo ya Tanzania.



Wananchi wametakiwa kuachana na dhana potofu kuwa chakula kinachopikwa kwa gesi ya LPG hakina ladha kama cha kupikwa kwa mkaa, huku ikielezwa kuwa tafiti zimebaini hakuna tofauti ya ubora wa chakula kinachopikwa kwa kutumia nishati hizo mbili.

Hayo yameelezwa na Afisa wa Ufundi wa Chama cha Wadau wa Gesi Tanzania TZLPGA, Mhandisi Huruma Msigwa, Mei 22, Jijini Dodoma, wakati akitoa elimu kwa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma UDOM kuhusu matumizi salama ya gesi ya LPG pamoja na fursa zilizopo katika sekta hiyo inayozidi kukua nchini.

Mhandisi Msigwa ametoa wito kwa jamii kuondokana na mtazamo potofu kuwa matumizi ya gesi ni hatari zaidi kuliko mkaa, akieleza kuwa ajali nyingi zinazohusishwa na gesi husababishwa na matumizi yasiyo sahihi pamoja na kukosa elimu ya matumizi salama ya nishati hiyo.

Kwa upande wake Mratibu wa Wanawake kwenye Sekta ya Gesi ya LPG kutoka TZLPGA Winner Joram Lukumay amesema tafiti zinaonyesha zaidi ya asilimia 90 ya Watanzania wanaotumia gesi ya LPG kupikia ni wanawake, jambo linaloonesha nafasi kubwa ya wanawake katika mapinduzi ya matumizi ya nishati safi nchini pamoja na mchango wao katika kulinda afya na mazingira.

Baadhi ya wanafunzi walioshiriki mafunzo hayo wameeleza kuwa mafunzo hayo yamewaongezea uelewa kuhusu sekta ya LPG, matumizi salama ya gesi pamoja na fursa za ajira na biashara zilizopo, huku wakiahidi kuendelea kutoa elimu hiyo kwa jamii ili kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Mafunzo hayo yaliyowashirikisha zaidi ya wanafunzi 120 kutoka kada mbalimbali za uhandisi na sayansi katika Chuo Kikuu cha Dodoma, yamelenga kuwaandaa vijana kuwa wataalamu na mabalozi wa matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini. 




Na Mwandishi Wetu 

KAMPUNI ya  DP World imetoa msaada wa ambulance kwa Idara ya Zimamoto na Usalama ya Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania(TPA) katika hafla ya makabidhiano iliyofanyika Bandari ya Dar es Salaam hivi karibuni. 

Ambulance hiyo itasaidia kuimarisha huduma za dharura za matibabu ndani ya bandari na kuwahudumia wadau wote wa bandari, wakiwemo wafanyakazi na wakandarasi wa DP World, wafanyakazi wa bandari, mabaharia pamoja na wageni.

Taarifa ya kampuni hiyo imeeleza kuwa mpango huo ni dhamira endelevu ya DP World katika kuimarisha afya na usalama, uimara wa shughuli za kiutendaji, pamoja na ustawi wa jamii ya bandari.




Mratibu wa Wanawake kwenye Sekta ya Gesi ya LPG kutoka Chama cha Wadau wa Gesi Tanzania TZLPGA Winner Joram Lukumay, amesema tafiti zinaonyesha zaidi ya asilimia 90 ya Watanzania wanaotumia  gesi ya LPG kupikia ni wanawake.

Hali inayodhihirisha nafasi kubwa ya wanawake katika mapinduzi ya matumizi ya nishati safi nchini pamoja na mchango wao katika kulinda afya na mazingira.

Akizungumza wakati wa mafunzo yaliyotolewa na Taasis hiyo kwa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) Mei 22, 2026 Jijini Dodoma , amewahamasisha vijana hususani wanawake kujitokeza kwa wingi kusoma taaluma zinazohusiana na sekta ya gesi.

Lukumay amesema licha ya wanawake kuwa watumiaji wakubwa wa nishati safi ya kupikia, bado idadi yao katika taaluma na ajira ndani ya sekta ya mafuta na gesi ni ndogo ukilinganisha na wanaume.

Amesema mafunzo hayo yamelenga kuwajengea wanafunzi maarifa na kuwaandaa kwa ajira pamoja na fursa za biashara katika sekta ya LPG ambayo inaendelea kukua nchini, huku akiwataka wanawake kujiamini na kupambana kuhakikisha wanapata uwiano sawa katika taaluma hiyo.

Aidha, amesema Serikali chini ya Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, imeendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia ikiwemo matumizi ya gesi ya LPG kwa wananchi na wafanyabiashara wadogo wa chakula maarufu kama mamalishe ili kulinda afya za wananchi pamoja na mazingira.

Kwa upande wake, Afisa wa Ufundi wa TZLPGA, Mhandisi Huruma Msigwa amesema elimu kuhusu matumizi salama ya gesi bado inahitajika kwa wananchi wengi ili kuondoa ajali za gesi ambazo mara nyingi husababishwa na matumizi yasiyo sahihi ya gesi.

Akitoa rai kwa jamii kuacha mila potofu ya kusema chakula kinachopikwa na gesi sio kitamu kama cha kupika kwenye mkaa, kwani tafiti zimefanyika na kubaini kuwa hakuna uhalisia wowote.

Baadhi ya wanafunzi walioshiriki mafunzo hayo wamesema yamewapa uelewa mkubwa kuhusu sekta ya LPG pamoja na fursa zilizopo, huku wakieleza kuwa yamewaongezea hamasa ya kujikita zaidi katika taaluma na shughuli zinazohusiana na nishati safi ya kupikia, pamoja kuhakikisha wanakuwa chachu kwa kuipeleka elimu hiyo kwa jamii.  

Katika mafunzo hayo zaidi ya wanafunzi 120 kutoka kada mbalimbali ikiwemo Shahada ya Science in Petroleum Engineering, Chemical and Processing Engineering, Mineral Processing Engineering pamoja na taaluma za Earth Sciences and Engineering kutoka College of Earth Sciences and Engineering (COESE) wamenufaika na mafunzo hayo.

Mafunzo hayo pia yamelenga kuunganisha maarifa ya darasani na mahitaji ya sekta ya mafuta na gesi kwa lengo la kuwaandaa wanafunzi kuwa wataalamu, wafanyabiashara na mabalozi wa matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini Tanzania.





Na Mwandishi Wetu

DIWANI wa Kata Zingiziwa iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Ilala jijini Dar es Salaam Salehe Kaniki ameendelea kugusa maisha ya makundi mbalimbali yenye uihitaji maalum.

Miongoni mwa makundi ambayo Diwani Kaniki ameyagusa na kuyafikia ni kundi la watu wenye mahitaji maalum ambapo leo Mei 22,2026 amekabidhi vitimwendo (baiskeli) viwili na viti vya kusukuma vitano na magongo kwa watu wenye ulemavu.

Akizungumza katika hafla ya kukabidhi msaada huo Diwani Kaniki amesema amefanikisha kufikisha msaada huo kwa walengwa kupitia ushirikiano kati yake na wenyeviti wa Serikali za mtaa katika kata hiyo kwa kuorodhesha walengwa na leo wamekabidhi msaada huo.

“Tumekutana kwa dhumuni moja la kusaidia ndugu zetu wenye uhitaji maalum ambao hawawezi kutembea ,tumekabidhi baiskeli mbili na viti vya kusukuma vitano kwa ujumla wake tumewafikia watu saba lakini tumetoa na magongo ya kutembelea.

“Kwahiyo kuna magongo mengine tumeweka ya ziada lakini kuna wengine wamejitokeza na tumeandika majina yao ambao nao tutawapatia.Kwangu msaada huu pia ni sehemu ya sadaka katika jamii kwani mwezi kama huu wa tano nilimpoteza kaka yangu.

“Kwahiyo msaada niliotoa leo iwe ni sehemu ya sadaka kwake huko aliko na iwe dua nzuri na Mwenyezi Mungu ampunguzie adhabu za kaburini,”amesema huku akisisitiza waliopata baiskeli hizo zitawarahisishia katika safari na wale waliokuwa wanabebwa sasa waaachwe watumie baiskeli hizo.

Wakati huo huo Diwani Kaniki ametumia nafasi hiyo kuishukuru Serikali inayoongozwa na Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kupeleka miradi ya maendeleo kwani kwenye Kata hiyo ya Zingiziwa limejengwa bweni kwa ajili ya wenye uhitaji maalum ambalo ni la kisasa na hivi karibuni litazinduliwa.

“Kwahiyo kuna wengine wanafunzi wenye mahitaji maalum hasa wenye ulemavu wataingia katika mabweni hayo kwa ajili ya kuwawezesha kupata elimu kwa uzuri zaidi .Hivyo namshukuru Rais Samia Suluhu Hassan na wakati huo huo namshukuru Mkuu wa Wilaya na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kwani fedha wanazotoa zinakwenda sehemu husika.”

Kwa upande wao baadhi ya waliopatiwa msaada huo akiwemo Pili Abdallah na Seif Mbedo wamemshukuru Diwani Kaniki kwa kuwapata msaada huo ambao unakwenda kutatua changamoto ya usafiri waliyokuwa wakiipata.





Imebainika kuwa changamoto zinazowakabili wauguzi katika Wilaya ya Bukombe zimepungua kwa kiasi kikubwa, kufuatia kupungua kwa malalamiko kutoka kwa watoa huduma na wapokea huduma katika kada ya afya.

Hayo yamebainika wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wauguzi Duniani, ambayo huadhimishwa kila tarehe 12 Mei. Wilaya ya Bukombe imeadhimisha siku hiyo Mei 22 mwaka huu.

Akizungumza katika maadhimisho hayo, Mkuu wa Wilaya ya Bukombe, Paskas Muragili, amesema kupungua kwa changamoto hizo kumetokana na juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita kuhakikisha huduma za afya zinaimarishwa nchini.

Mhe. Muragili amefafanua kuwa serikali imeendelea kuboresha mazingira ya kazi kwa wauguzi, ikiwemo kuongeza watumishi na vifaa tiba, hatua iliyosaidia kupunguza mzigo wa kazi na malalamiko.

Katika hatua nyingine, DC Muragili amesema kuwa jumla ya wauguzi 165 wameajiriwa katika mwaka wa fedha wa 2025/2026. Amemuagiza Mganga Mkuu wa Wilaya ya Bukombe kuhakikisha anawapangia vituo waajiriwa hao wapya kwa uwiano.

Amesisitiza kuwa lengo ni kuhakikisha kila kituo cha kutolea huduma za afya wilayani humo kinaondokana na uhaba wa wauguzi na wananchi wanapata huduma bora kwa wakati.

Kwa upande wake, Muuguzi Mkuu wa Wilaya ya Bukombe, Diana Makubi, amesema malalamiko ya wauguzi na wagonjwa yamepungua kwa kiasi kikubwa. Amesema hii inatokana na uanzishwaji wa madawati maalumu yanayoshughulikia changamoto za wauguzi.

Chama cha Wauguzi Wilayani Bukombe kimekuwa kikiadhimisha Siku ya Wauguzi Duniani kwa miaka minne mfululizo. Lengo ni kuwatia nguvu na kuwapa hamasa wauguzi kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi na ufanisi.





 


Taasisi ya Saratani Ocean Road imeshiriki katika uzinduzi wa jukwaa la utoaji huduma za afya na bima zinazofanyika katika viwanja vya Posta-TTCL Kijitonyama.

Jukwaa hilo linalenga kuimarisha juhudi za serikali katika kuboresha afya kwa kutoa elimu ya afya kwa jamii.

Pia kuhamasisha kinga dhidi ya magonjwa mbalimbali pamoja na kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa kujiunga na huduma za bima ya afya.

Taasisi ya saratani ocean road imepata fursa ya kutoa elimu ya saratani mbalimbali na kuwafanyia uchunguzi wa saratani ya matiti na saratani ya tezi dume kwa wananchi waliofika katika viwanja hivyo.

Aidha taasisi hiyo imewataka wananchi kufika katika viwanja hivyo kupata elimu na kuchunguzwa afya zao bila malipo yoyote.

Jukwaa hilo la utoaji huduma za afya na bima limeanza tarehe 20/05/2026 na linatarajia kumalizika tarehe 24/05/2026.

NA Janeth Raphael MichuziTv Bungeni Dodoma.

Mbunge wa Katavi, Thomas Maganga ameipongeza Wizara ya Viwanda na Biashara kwa kile alichodai kuwa ni kazi kubwa na nzuri inayofanywa katika kukuza sekta ya biashara na uwekezaji nchini, huku akimtaka Waziri wa wizara hiyo, Judith Kapinga kuweka nguvu zaidi katika kulinda wafanyabiashara wa ndani dhidi ya ushindani kutoka kwa wafanyabiashara wa kigeni.

Akichangia hoja ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Viwanda na Biashara kwa mwaka wa fedha 2026/2027 leo Bungeni jijini Dodoma, Maganga alisema historia itamkumbuka Waziri Kapinga iwapo atasimamia kwa uthabiti maslahi ya wafanyabiashara wazawa na kuhakikisha wanapata mazingira rafiki ya kufanya biashara na kuwekeza nchini.

“Dada yangu hakuna kitu ambacho taifa litakukumbuka kama kulinda wafanyabiashara wa ndani,” alisema Maganga huku akisisitiza kuwa ukuaji wa uchumi wa taifa unapaswa kuwanufaisha zaidi Watanzania wenyewe.

Mbunge huyo amesema ipo haja ya Serikali kuweka mifumo madhubuti ya kudhibiti ongezeko kubwa la wafanyabiashara wa kigeni wanaoingia nchini na kufanya shughuli ambazo zinaweza kufanywa na wazawa, akieleza kuwa hali hiyo imekuwa changamoto kwa wafanyabiashara wengi wa ndani kushindana kwenye soko.

Amesema pamoja na umuhimu wa uwekezaji kutoka nje ya nchi, Serikali inapaswa kuweka mkazo mkubwa katika kuwajengea uwezo wawekezaji wa ndani ili waweze kuwa nguzo ya uchumi wa taifa kwa muda mrefu.

Katika mchango wake huo, Maganga pia aliwataka wafanyabiashara na wawekezaji wa Kitanzania kutumia fursa zilizopo kuwekeza zaidi ndani ya nchi, akisema hatua hiyo inaweza kusaidia kupunguza tatizo la ajira kwa kiwango kikubwa katika miaka michache ijayo.

“Wawekezaji wa ndani wakiamua kuwekeza kwa nguvu nchini, naamini ndani ya miaka mitano ijayo changamoto ya ukosefu wa ajira itapungua kwa kiasi kikubwa,” alisema.

Aidha, Maganga ameeleza kuwa baadhi ya wawekezaji wa kigeni wamekuwa wakinufaika zaidi na rasilimali na fursa za ndani bila kuacha manufaa makubwa kwa taifa, hali inayozua mjadala kuhusu namna bora ya kusawazisha uwekezaji wa ndani na wa nje.

“Hao wawekezaji wa nje wanakuja na fedha kidogo lakini wakishafanikiwa wanaondoka na faida kubwa, wakati mwingine wakituachia changamoto mbalimbali katika jamii,” alisema.

Kauli ya mbunge huyo imeibua mjadala kuhusu umuhimu wa Serikali kuendelea kuweka sera na mikakati itakayowezesha wafanyabiashara wa ndani kukua, kuhimili ushindani wa soko na kuchangia kikamilifu katika maendeleo ya uchumi wa nchi.

Wizara ya Viwanda na Biashara imekuwa ikiwasilisha bungeni mikakati mbalimbali inayolenga kukuza viwanda vya ndani, kuongeza uzalishaji wa bidhaa za Kitanzania pamoja na kuvutia uwekezaji wenye tija kwa taifa.



Na Janeth Raphael MichuziTv Bungeni Dodoma 

Serikali kupitia Wakala wa Vipimo (WMA) imeendelea kuimarisha huduma za uhakiki wa vipimo nchini kwa kukamilisha ujenzi wa Kituo cha Kisasa cha Uhakiki kilichopo eneo la Misugusugu, mkoani Pwani, ambacho kimegharimu jumla ya shilingi bilioni 7.3.

Kituo hicho kilichojengwa katika eneo lenye ukubwa wa hekta 2.4 ni sehemu ya utekelezaji wa mkakati wa Serikali wa kusogeza karibu huduma za vipimo kwa wananchi na wadau wa kibiashara, sambamba na kuimarisha miundombinu ya kitaifa ya udhibiti wa ubora wa vipimo.

Kwa mujibu wa taarifa iliyowasilishwa Bungeni, kituo hicho kitahusika na uhakiki wa vifaa mbalimbali vinavyotumika katika sekta za nishati na maji, ikiwemo matenki ya magari yanayosafirisha vimiminika, mita mpya za umeme pamoja na dira za maji kabla ya kufungwa kwa watumiaji.

Lengo kuu la uhakiki huo ni kuhakikisha kuwa vifaa hivyo vinakidhi viwango vilivyowekwa kitaifa na kimataifa, na hivyo kuhakikisha usahihi wa vipimo, kulinda haki za watumiaji na wauzaji, pamoja na kuongeza ufanisi katika usimamizi wa rasilimali za umma.

Hata hivyo, WMA imebainisha kuwepo kwa changamoto mbalimbali zinazokwamisha utekelezaji wake, ikiwemo mwitikio hafifu kutoka kwa baadhi ya wazabuni wa mita za umeme kushindwa kutekeleza takwa la kisheria la kuwasilisha mita hizo kwa ajili ya uhakiki kabla ya kusambazwa kwa taasisi nunuzi.

Changamoto nyingine ni malimbikizo ya muda mrefu ya madai ya malipo ya huduma za uhakiki wa dira za maji kutoka kwa baadhi ya kampuni zilizopewa zabuni, hali inayoweza kuathiri uendelevu wa huduma na ufanisi wa taasisi hiyo.

Akizungumza Bungeni, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo, Mariam Ditopile, amesema kamati yake imebaini hatua nzuri zilizofikiwa na WMA katika kuboresha huduma zake, ikiwemo ujenzi wa kituo hicho cha kisasa cha Misugusugu.

Ditopile amesema kuwa kamati imepongeza juhudi za Serikali katika kuimarisha miundombinu ya uhakiki wa vipimo, lakini pia imesisitiza umuhimu wa kuongeza ufuatiliaji wa wazabuni ili kuhakikisha wanazingatia matakwa ya kisheria kabla ya kusambaza vifaa kwa wananchi.

Aidha, alibainisha kuwa changamoto ya malimbikizo ya madeni ya huduma za uhakiki inapaswa kushughulikiwa kwa haraka ili kuepusha athari katika uendeshaji wa taasisi na utekelezaji wa majukumu yake ya msingi.

Kamati hiyo pia imeitaka Serikali kuendelea kuimarisha usimamizi wa sekta ya vipimo ili kuhakikisha vifaa vyote vinavyotumika nchini vinakuwa sahihi na vinakidhi viwango vilivyowekwa, hatua itakayosaidia kuongeza ufanisi katika sekta mbalimbali za uchumi.

Kwa ujumla, ujenzi wa Kituo cha Misugusugu unatajwa kuwa hatua muhimu katika mageuzi ya sekta ya vipimo nchini, ukiwa na lengo la kuongeza uwazi, usahihi na ulinzi kwa watumiaji wa huduma mbalimbali za kijamii na kiuchumi.




Top News