Mkuu wa Mkoa Dodoma Mhe Rosemary Senyalume ametoa wito kwa Wananchi wote wa Mkoa Dodoma kujitokeza kutumia fursa ya kutoa kero zao na kupata utatuzi katika siku 3 zilizoandaliwa kuanzia tarehe 4 hadi 6 Machi 2026 katika viwanja vya Nyerere Square kwani Taasisi zote za Umma zitakuwepo hapo kwaajili ya jambo hilo.

Mhe Senyamule ameyasema hayo leo Jijini Dodoma Machi 2,2026 wakati akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu jambo waliloandaa la utatuzi wa kero mbalimbali za wananchi wa Dodoma kama ambavyo yamekuwa ni maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan, maelekezo ya vitendo ya Waziri Mkuu Dkt Mwigulu Nchemba na maelekezo mahsusi ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI Prof.Riziki Shemdoe ambayo yamekuwa yakisisitiza utatuzi wa kero za Wananchi.

"Taasiisi zote za Umma zilizopo katika Mkoa wa Dodoma zitakuwepo pale Nyerere Square kwa siku tatu kusikiliza nakutatua kero za wananchi,kwahiyo ni wito wangu kwa wananchi wa Mkoa wa Dodoma kujitoleza kuja kutumia fursa hii adhimu ambayo tumeiweka ili kuwarahishia kwani Taasisi zitakuwepo pale kutoka upande wa afya,maji na hata miundombinu".

Aidha Mkuu wa Mkoa huyo ameainisha huduma tatu muhimu zitakazotolewa katika viwanja hivyo kwa siku hizo 3, kuwa ni kusikiliza  kero za wananchi ambapo Taasisi zote za Umma zitashiriki kazi hii Pia kutoa Taarifa kwa Umma wa Wana Dodoma na Taifa kwa ujumla juu ya kazi iliyofanywa katika siku 100 za Dkt Samia akiwa madarakani katika awamu ya sita na muhula wake pili.

Ambapo tatu ni utoaji wa huduma bure kwa wananchi kama vile upimaji wa magonjwa ikiwemo sukari na presha pamoja na kuwepo kwa huduma za ki hiari za kutoa damu kwa watakaopenda ambapo huduma hizi zimeunganiswa ili kuwa fursa kwa wananchi wakati wa utatuzi wa kero zao.

Pamoja na hayo pia ametoa wito kwa Taasisi za Umma na Watumishi wake katika Mkoa wa Dodoma kuhakikisha kwamba kila mmoja anawajibika kusikiliza kero za wananchi kwani kama Mkoa wanategemea kutengeneza mfumo kuanzia ngazi za chini za Vitongoji mpaka ngazi ya Mkoa, mfumo wa kupata Taarifa za kero zinazosikilizwa na utatuzi wake katika ngazi zote na kuzitolea Taarifa kila mwezi.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa -TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amewaelekeza Wakuu wa Mikoa wote nchini kuzisimamia Halmashauri zao kuhakikisha zinaweka siku maalum ya kusikiliza malalamiko na kero za wananchi katika ngazi ya kata ili kurahisisha upatikanaji wa huduma na ufumbuzi wa changamoto kwa wananchi wa ngazi ya chini.

Maelekezo hayo ameyatoa Machi 2, 2026 wakati akifungua Mkutano Mkuu wa 12 wa Umoja wa Maafisa Elimu wa Mikoa na Halmashauri Tanzania Bara unaofanyika katika Ukumbi wa Lush Garden Hotel jijini Arusha, ambapo amesisitiza kuwa ni muhimu kwa Mkurugenzi wa Halmashauri na Timu ya Usimamizi wa Halmashauri (CMT) kuwa karibu na wananchi na kusikiliza kero zao mapema badala ya kusubiri ziibuliwe wakati wa ziara za viongozi wakuu wa kitaifa.

Amesema kukosekana kwa utaratibu wa kuwasikiliza wananchi katika ngazi ya halmashauri kumesababisha wananchi wengi kujitokeza na malalamiko wakati wa ziara za viongozi wa kitaifa, hususan ziara ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, inayoendelea katika mikoa mbalimbali nchini.

Aidha, Prof. Shemdoe amewaelekeza Maafisa Elimu wa Mikoa na Halmashauri kusimamia kikamilifu changamoto ya mmomonyoko wa maadili katika jamii, akisisitiza kuwa mwalimu ni kioo cha jamii na ana jukumu la kutoa malezi na mafundisho yatakayojenga maadili mema kwa wanafunzi.

Ameongeza kuwa katika kipindi hiki cha ukuaji wa kasi wa sayansi na teknolojia, walimu wanapaswa kuwafundisha wanafunzi matumizi sahihi ya TEHAMA, hususan katika mitandao ya kijamii, ili teknolojia iwe chachu ya kuimarisha maadili na si kuyadhoofisha.

Wakati huo huo, Prof. Shemdoe amewasisitiza Maafisa hao kuhakikisha kuwa wanafuatilia kwq karibu na kutekeleza maagizo yaliyotolewa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba ya kuhakikisha ndani ya miezi sita kila shule nchini kunakuwa na vyoo vya kutosha vya wanafunzi na walimu.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Elimu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI, Atupele Mwambene, amesema Mkutano Mkuu huo wa 12 umebeba kaulimbiu isemayo “Matumizi ya TEHAMA ni Nguzo Muhimu ya Uboreshaji wa Elimu Tanzania” na unalenga kufanya majadiliano yenye tija yatakayoboresha na kuimarisha sekta ya elimu nchini.











Na WAF-Korogwe

Mganga Mkuu wa mkoa wa Tanga Dkt. Japhet Simeyo amesema kikao kazi cha tathmini ya matukio na athari za kiafya kitawajengea uwezo wataalam kwenye mkoa huo ili wawe tayari kuzuia na kukabiliana na majanga yatokanayo na dharura.

Dkt. Simeyo ameyasema hayo kwa niaba ya Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga leo Machi 02, 2026 katika kikao kazi cha tathmini ya matukio na athari za kiafya katika mkoa wa Tanga, kilichoandaliwa na Wizara ya Afya kwa kushirikiana na asasi isiyo ya kiserikali ya PATH& CIHEB.

"Mkoa wa Tanga umekuwa na Majanga mbalimbali yanayotokea ikiwa ni pamoja na moto, ajali za barabarani, Magonjwa ya Milipuko na mabadiliko ya Tabianchi" amesema Dkt.Simeyo na kuongeza

"Mafunzo haya yamekuja kwa wakati muafaka kwani yatawajengea uwezo baina ya sekta mtambuka kwa kupitia za majanga yaliyowahi kutokea na kuimarisha afua za udhibiti wa majanga hayo kabla hayajatokea"  amesema Dkt Simeyo

Kwa upande wake Mratibu-Udhibiti Athari za Majanga Wizara ya Afya, Dkt Saumu Nungu amesema kuwa kikao kazi hicho kinalenga kuainisha athari ambazo zinaweza kusababisha majanga na dharura katika mkoa wa Tanga na kuandaa mpango kazi ambao utasaidia mkoa kujiandaa vizuri.

"Pamoja na hilo kikao kupitia kikao hiki tutandaa kalenda itakayokuwa inaonyesha wakati ambao majanga yanaweza kutokea yaani Tanga Region Health Profile Risk and Calendar" amesema Dkt Saumu

Amefafanua kuwa kupitia kalenda ya matukio, timu za kukaliana na majanga ya dharura zitaweza kujiandaa mapema kabla ya kipindi ambacho athari hizo zina uwezekano wa kutokea, hivyo kuleta tija na kulinda afya za wananchi dhidi ya athari za majanga hayo.

Naye Dkt. Said Sheuya kutoka PATH&CIHEB amesema kuwa, Taasisi hiyo imekuwa ikishirikiana na Wizara ya Afya katika nyanja mbalimbali ikiwa ni pamoja na mapambano ya magonjwa ya mlipuko na ufuatiliaji wa magonjwa, ushirikiano wa mfumo wa Afya Moja, kuhakikisha uwepo wa mifumo ya afya inayosomana katika utoaji wa taarifa za magonjwa, na kufanya mafunzo kwa timu za kupambana na dharura katika mikoa.







Na mwandishi wetu, Arusha.

Serikali imehamasisha  mapambano dhidi ya VVU na UKIMWI kwa kundi la vijana katika  Chuo cha Uhasibu Arusha  (IAA) na Taasisi ya Maendeleo ya Jamii ya Tengeru.

Hamasa hiyo imetolewa leo 02 Machi 2026, na Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge Uratibu na Wenye Ulemavu Mhe. Ummy Nderiananga katika  ziara yake ya  kufuatilia na kutathimini utekelezaji wa Afua za VVU na UKIMWI katika vyuo vya kati na Vyuo Vikuu Jijini Arusha.

Mhe. Nderiananga, ameipongeza Tume ya kudhibiti UKIMWI  Tanzania (TACAIDS)  kwa kazi kubwa ya kusimamia utekelezaji wa Afua za VVU na UKIMWI waliofanya kwenye Taasisi 26 za vyuo vya kati na Vyuo Vikuu nchini, na kuwapongeza vijana wa Vyuo hivyo kwa  kupambana nakuchukua tahadhali na kuzungatia elimu  ya kinga na maambukiz ya Virusi vya UKIMWI waliyoipata kupitia wataalam mbalimbali. 

Pia, Mhe. Nderiananga amesisitiza kundi la vijana haswa wa Kiume kuhamasika katika upimaji ili watambue hali za Afya zao na kuhimiza Ufuasi mzuri wa Dawa za kufubaza virusi vya UKIMWI kwa waathirika wapya, lakini pia amewapongeza Waathirika wote wa VVU  kote nchini kwa matumizi sahihi ya ARV.

Awali, Mkurugenzi wa Idara ya Mwitikio wa Kitaifa wa UKIMWI kutoka Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS) Bi Audrey Njelekera, Amesema kuwa Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali kupitia takwimu zilizopo inamipango madhubuti ya kupunguza na kutokomeza maambukizi ya VVU na UKIMWI nchini kote.

Ameongeza kuwa, takwimu zinaonyesha kuwa kundi la vijana kuanzia miaka 15 hadi 24 ndio linaloathirika zaidi na maambukizi mapya hivyo TACAIDS imeanzisha  Klabu za kijamii kwenye vyuo vya kati na vikuu ili kusaidia  kupunguza unyanyapaa, kuongeza idadi ya wanafunzi kupima na kuongeza ushiriki wa wanafunzi katika mapamabano dhidi ya VVU. Vilevile, kuanzisha programu mbalimbali za kuhamasisha na kuelimisha kupitia mijadala, kuandika machapisho,  vibonzo, picha mjongeo na kampeni za kwenye mitandao ya kijamii.

Nae, Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Mipango, Fedha na Utawala wa  Chuo cha Uhasibu Arusha, Dkt. Eliakira Nnko amesema kuwa, Chuo kinaendelea kuweka  mipango na mikakati ya utekelezaji wa Afua za UKIMWI mahali pakazi  kwa watumishi na wanafunzi wanaoishi na maambukizi ya virusi vya UKIMWI, lengo kuu ni kuhakikisha Wanafunzi na watumishi wanabaki na Afya njema, Kupunguza vifo na kutokomeza unyanyapaa ili kuimarisha utendaji kazi na kuweka  mazingira salama kwa watumishi na  wanafunzi.



 

Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, ameiomba Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kusimamia kikamilifu utoaji wa hati za ardhi ili kuhakikisha zinazingatia taratibu na mipango miji, akisema kuwa uzembe katika mchakato huo unachangia kuongezeka kwa migogoro ya ardhi.
Akizungumza jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa programu ya Samia Ardhi Kliniki, Mpogolo alisema baadhi ya hati zimekuwa zikitolewa bila kuzingatia ramani na mpangilio rasmi wa maeneo, hali inayosababisha wananchi kujenga katika maeneo yasiyoruhusiwa ikiwemo kuziba barabara.

“Tusipofuata taratibu za upangaji miji, tutazalisha migogoro mikubwa katika jamii. Watu wanajikuta wanaziba barabara au kujenga katika hifadhi za wazi kwa sababu ya makosa ya kiutendaji,” alisema Mpogolo.

Aidha, aliwataka wananchi wa Mkoa wa Dar es Salaam kujitokeza kwa wingi kushiriki katika Samia Ardhi Kliniki ili kupata huduma mbalimbali zinazotolewa na Wizara ya Ardhi, ikiwemo ushauri wa kitaalamu, uhakiki wa nyaraka, pamoja na utatuzi wa migogoro ya ardhi.

Katika hatua nyingine, Mpogolo ameipongeza Wizara ya Ardhi kwa kuanzisha kliniki hiyo, akieleza kuwa itasaidia kupunguza malalamiko ya muda mrefu na kuimarisha uwazi pamoja na uwajibikaji katika sekta ya ardhi.

Aliongeza kuwa ushirikiano kati ya serikali na wananchi ni muhimu katika kuhakikisha mipango miji inaheshimiwa na maendeleo yanafanyika kwa utaratibu unaokubalika kisheria.
Naibu Katibu Mkuu Bi. Lucy Kabyemera akimkabidhi hati Miliki ya Ardhi Mkuu wa Wilaya ya Ilala Bw. Edrward Mpogolo katika tukio la uzinduzi wa Samia Ardhi Kliniki jijini Dar es Salaam tarehe 2 Machi 2026. Kushoto ni Mkurugenzi wa Kitengo cha Milki Wizara ya Ardhi Dkt Upendo Matotola
* Huku Nchi za Afrika zikitakiwa kufanya biashara za pamoja, Wananchi waitwa kutoa maoni…

Na Leandra Gabriel, MMG

KATIKA Kuhakikisha biashara, uwekezaji na uchumi wa Nchi unakua Serikali kwa kushirikiana na sekta binafsi na wadau mbalimbali wa Maendeleo wameendelea kujadili, kutoa maoni na mapendekezo yatakayowezesha kuweka mazingira mazuri ya biashara na uwekezaji pamoja na kuiandaa jamii kuona wadau wa maendeleo ni wadau wakubwa katika kuyafikia maendeleo hayo.

Akizungumza leo katika ukumbi wa Johari Rotana Jijini Dar es Salaam Katika mkutano wa Uhakiki wa Mpango wa Pili wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji (MKUMBI II) Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Prof. Kitila Mkumbo amesema, kuelekea utekelezaji wa Dira 2050 Serikali imekamilisha maandalizi ya rasimu ya mkakati wa pili wa kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini ‘ MKUMBI’ na hatua inayofuata ni kuwarudishia wadau waliotoa maoni waone namna gani maoni yao yamezingatiwa.

"Katika kuhakiki maoni hayo yaliyotolewa na wadau mbalimbali leo tumekutana na Mabalozi wanaoziwakilisha Nchi mbalimbali hapa Nchini na wawakilishi wa mashirika ya Kimataifa ambao wapo hapa Dar es Salaam na Dodoma wamepitia nyaraka hizi na tutawafikia wadau wengi zaidi wakiwemo wakuu wa mikoa, makatibu Tawala na wakurugenzi wa Halmashauri kwa Kuwa masuala mengi yatatekelezwa katika ngazi ya Serikali za Mitaa.’’ Ameeleza.

Prof. Kitila amesema kuwa rasimu ya mpango huo hiyo imebainisha maeneo kumi na moja ambayo yanahitaji kufanyiwa kazi pamoja na changamoto 59 zilizoibuliwa na wataalam ambazo zinakwaza biashara na uwekezaji na wamependekeza hatua za kimageuzi 246.

Ametaja maeneo kumi na moja ambayo yanahitaji kufanyiwa kazi pamoja na mazingira ya kuanzisha biashara, maeneo ya kufanyia biashara, mitaji, mazingira ya kidijitali, ustadi, mafunzo na utafiti, masoko, miundombinu ya huduma, utatuzi wa migogoro, ulinzi wa Hakimiliki, kubadili mitazamo na uwajibikaji pamoja na usimamizi, ufuatiliaji na upimaji.

Aidha amehimiza Bara la Afrika kukuza ushirikiano katika biashara hususani katika masoko na biashara za pamoja na kuwa timu moja kupitia Jumuiya zao ikiwemo ya Afrika Mashariki na SADC na kutumia vizuri soko la pamoja ambalo biashara hufanyika kwa asilimia 16 pekee.

Kuhusiana na ushiriki wa wananchi katika kufanikisha Dira ya Maendeleo 2050 Waziri Kitila amesema baada ya kukamilishwa kwa rasimu wanaiweka hadharani ili wadau na wananchi waweze kutoa maoni yao kupitia tovuti ya Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji http://www.popi.go.tz ili kuboresha rasimu hiyo kabla ya haijaingizwa kwenye mchakato wa kufanya maamuzi ndani ya Serikali na kusisitiza kuwa kufikia mwezi wa nne itaingizwa rasmi katika mchakato wa kufanya maamuzi ndani ya Serikali na baadaye kuidhinishwa rasmi.

Awali Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Uwekezaji na Mipango Dkt. Fred Msemwa alieleza kuwa licha ya Tanzania kutajwa katika ukuaji wa uchumi kukamilika kwa mpango huo kutachochea zaidi ukuaji wa uchumi, ajira, uboreshwaji wa mazingira ya ufanyaji biashara na uwekezaji pamoja na kuandaa Sera, Sheria na Mipango ya kuhakikisha sekta binafsi zinafanya kazi katika mazingira rafiki huku watanzania wakinufaika na uwekezaji huo na pato la Taifa kwa ujumla likiendelea kukua.

Mkutano huo umeikutanisha Serikali, Mabalozi wanaowakilisha Nchi mbalimbali zikiwemo Zambia, Ujerumani, Marekani, Vietnam, Comoro, mwakilishi wa Jumuiya ya Umoja wa Ulaya, Italia na Hispania ambao kupitia nyaraka zilizowasilishwa kwao walitoa maoni na wamekubali mapendekezo hayo kwa kueleza kuwa yatasaidia sana iwapo yatatekelezwa.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Prof. Kitila Mkumbo akizungumza wakati wa mkutano huo na kueleza kuwa, kuelekea utekelezaji wa Dira 2050 Serikali imekamilisha maandalizi ya rasimu ya mkakati  wa pili wa kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini ´Mkumbí  na hatua inayofuata ni kuwarudishia wadau waliotoa maoni waone  namna gani maoni yao yamezingatiwa. Leo jijini Dar es Salaam.
Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Uwekezaji na Mipango Dkt. Fred Msemwa akizungumza wakati wa mkutano huo na kueleza kuwa licha ya Tanzania kutajwa katika ukuaji wa uchumi kukamilika kwa mpango huo kutachochea zaidi ukuaji wa uchumi, ajira, uboreshwaji wa mazingira ya ufanyaji biashara. Leo jijini Dar es Salaam.
Prof. Faustine Kamuzora, Katibu wa Timu ya Kitaifa ya Kiufundi (NTT) akizungumza katika mkutano huo.

Matukio mbalimbali wakati wa Mkutano wa Uhakiki wa Mpango wa Pili wa kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji (MKUMBI II.)


Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) kwa kushirikiana na Wizara ya Mifugo na Uvuvi imezindua rasmi Vituo 23 vya Kukusanyia Maziwa (MCCs) vilivyojengwa na kuboreshwa kupitia Mradi Shirikishi wa Wasindikaji na Wazalishaji wa Maziwa Tanzania (TI3P), hatua inayolenga kuimarisha mnyororo wa thamani wa maziwa na kuongeza tija kwa wafugaji nchini.

Uzinduzi huo wa kitaifa umefanyika katika Kituo cha Kukusanyia Maziwa cha Nshamba, Wilaya ya Muleba, mkoani Kagera, ukiongozwa na Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Bashiru Ally Kakurwa.

Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri amesema mradi wa TI3P umeleta mageuzi chanya katika sekta ya maziwa kwa kuongeza uzalishaji, kuboresha ubora wa maziwa na kupanua fursa za masoko kwa wafugaji wadogo, wa kati na wakubwa. Alieleza kuwa vituo vya kukusanyia maziwa ni miundombinu ya kimkakati inayowezesha uhifadhi wa maziwa katika viwango vinavyokubalika, kupunguza upotevu wa mazao na kuongeza thamani kabla ya usindikaji.

Mradi wa TI3P unafadhiliwa na Gates Foundation na kutekelezwa na TADB kwa kushirikiana na Heifer International Tanzania pamoja na Land O’Lakes Venture37, ukiwa na lengo la kuwaunganisha wazalishaji na wasindikaji katika mfumo jumuishi na endelevu.

Mafanikio ya Utekelezaji

Akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi huo, Mkurugenzi Mwendeshaji wa TADB, Frank Nyabundege, amesema tangu kuanza kwake, TI3P umewezesha utolewaji wa zaidi ya Shilingi bilioni 41 kama mikopo kwa wadau wa sekta ya maziwa.

Amesema mitamba 3,254 yenye thamani ya Shilingi bilioni 10.8 imenunuliwa ili kuongeza uzalishaji, huku viwanda 15 vya usindikaji vikifadhiliwa kwa zaidi ya Shilingi bilioni 22, hatua iliyoongeza uwezo wa kitaifa wa uchakataji wa maziwa.

Kwa mujibu wa Nyabundege, wafugaji 92,831 wamefikiwa moja kwa moja kupitia huduma za kifedha, mafunzo na huduma za ugani, huku ruzuku fungamanifu (Matching Grants) ya Shilingi bilioni 1.448 ikitolewa kwa wazalishaji na wasindikaji.

Aidha, vyama 45 vya wazalishaji wa maziwa (FPOs) vimeanzishwa na kuimarishwa, vikikusanya wastani wa lita 19,047 kwa siku. Vituo 23 vilivyojengwa na kuboreshwa katika Kanda ya Ziwa, Nyanda za Juu Kusini na Zanzibar vina uwezo wa kukusanya lita 45,500 kwa siku, vikihudumia wafugaji 4,016 katika mikoa nane na wilaya 18.

Ziara ya Miradi Mkoani Kagera

Katika ziara yake mkoani Kagera, Waziri alitembelea Chama cha Ushirika cha Maruku, Bukoba Mjini, na kushuhudia utekelezaji wa mpango wa “Kopa Ng’ombe, Lipa Maziwa” unaolenga kuongeza kipato kwa vijana na wanawake.

Kupitia chama hicho chenye wanachama 118, wanachama 24 wamenufaika na mitamba 24 yenye mimba pamoja na ruzuku ya Shilingi milioni 18 kupunguza mzigo wa marejesho ya mikopo. Pia kituo hicho kimekarabatiwa kwa zaidi ya Shilingi milioni 10.4 na kupatiwa tanki la kuhifadhia maziwa la lita 2,000. Wafugaji hao wameunganishwa na soko la uhakika la Kahama Fresh Limited.

Katika Kituo cha Nshamba chenye wanachama 541, TADB imewezesha uanzishwaji wa MCC yenye uwezo wa kukusanya lita 2,000 kwa siku pamoja na jenereta ya dharura. Aidha, katika Ushirika wa UWAWAMA wilayani Karagwe, wanachama 76 wamenufaika na mitamba 110 yenye mimba na ruzuku ya Shilingi milioni 85 kupunguza marejesho ya mikopo.

Mwelekeo wa Serikali

Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan imeendelea kuweka mazingira wezeshi kwa uwekezaji katika sekta ya mifugo kwa lengo la kuongeza thamani ya mazao ya mifugo, kukuza ajira na kuinua kipato cha wananchi vijijini.

TADB imesisitiza kuwa itaendelea kushirikiana na Serikali, washirika wa maendeleo na sekta binafsi ili kuhakikisha mafanikio ya mradi wa TI3P yanaimarisha uchumi wa viwanda unaotegemea uzalishaji bora na ushiriki mpana wa wafugaji katika mnyororo wa thamani wa maziwa.







Na Humphrey Shao,Michuzi Tv

Dar es Salaam, Machi 2, 2026 – Serikali imetangaza kuwa kesho, Machi 3, 2026, kutafanyika hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi kwa ajili ya ujenzi wa matanki 15 ya kuhifadhia mafuta katika Bandari ya Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya mpango mkubwa wa kupanua na kuboresha bandari hiyo kama lango kuu la biashara nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa, amesema mgeni rasmi katika hafla hiyo anatarajiwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ambaye ataongoza tukio hilo muhimu kwa maendeleo ya sekta ya uchukuzi na uchumi wa taifa kwa ujumla.

Profesa Mbarawa amesema ujenzi wa matanki hayo unaonesha dhamira thabiti ya Serikali ya Awamu ya Sita katika kuimarisha miundombinu ya kimkakati itakayoongeza ufanisi wa Bandari ya Dar es Salaam katika kuhudumia meli za mafuta na kuiweka miongoni mwa bandari zenye ushindani mkubwa katika ukanda wa Bahari ya Hindi.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, mradi wa ujenzi wa matanki 15 unatarajiwa kukamilika mwezi Februari 2027, ambapo yatakuwa na uwezo wa kupokea shehena ya mafuta ya mita za ujazo 378,000 kwa wakati mmoja. Hatua hiyo itawezesha bandari kuhudumia meli kubwa za mafuta na kupunguza muda wa meli kukaa nangani kutoka siku 10 hadi siku 3 kwa meli zenye ujazo wa tani 150,000.

Amesema kukamilika kwa mradi huo kutavutia meli nyingi zaidi za mafuta kutumia Bandari ya Dar es Salaam, kupunguza foleni ya meli, kuongeza ufanisi wa utoaji huduma na kuimarisha usalama wa nishati nchini.

Kwa sasa, bandari hiyo ina matanki yanayomilikiwa na wadau wengine yenye uwezo wa mita za ujazo 1,051,888.52. Utekelezaji wa mradi huu utaongeza uwezo wa kupokea mafuta hadi kufikia mita za ujazo 1,429,888.52, na kuifanya bandari hiyo kuwa kitovu cha biashara kwa nchi za Kusini, Kati na Mashariki mwa Afrika.

Sambamba na uimarishaji wa bandari, Serikali inaendelea kuboresha miundombinu ya reli ikiwemo ukarabati wa reli ya MGR, kukamilisha ujenzi wa Reli ya Kisasa ya SGR pamoja na kuboresha reli ya TAZARA kwa ushirikiano na sekta binafsi. Kupitia reli hizo, shehena itakayohudumiwa bandarini itasafirishwa hadi maeneo mbalimbali ndani na nje ya nchi, hatua itakayopunguza msongamano wa mizigo bandarini na wa malori katika Jiji la Dar es Salaam, kupunguza gharama za usafirishaji na kuongeza ufanisi katika mnyororo wa ugavi.

Profesa Mbarawa amewahimiza wadau wa sekta ya uchukuzi kuendelea kushirikiana na Serikali kwa kuwekeza katika miundombinu ya kisasa na vifaa vya usafirishaji ili kuongeza kasi ya uondoshaji mizigo bandarini na kuimarisha ushindani wa taifa.

Aidha, amewakaribisha wanahabari, wadau wa usafirishaji, wananchi wa Mkoa wa Dar es Salaam na mikoa jirani kushiriki katika tukio hilo ambalo amelitaja kuwa la kihistoria na lenye umuhimu mkubwa kwa maendeleo ya nchi.




Na Mwandishi wa OMH

Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, amefanya mazungumzo na Bw. Keith Liddell, Mwanzilishi na Mwenyekiti wa kampuni ya Lifezone Metals Limited, inayomiliki Tembo Nickel Corporation Limited kwa ubia na Serikali ya Tanzania kupitia Ofisi ya Msajili wa Hazina.

Mazungumzo hayo yalifanyika Jumatatu, Machi 2, 2026, katika Ofisi ya Msajili wa Hazina jijini Dar es Salaam, yakilenga kujadili maendeleo ya utekelezaji wa Mradi wa Kabanga Nickel uliopo mkoani Kagera, ambao thamani ya uwekezaji wake unakadiriwa kuwa zaidi ya dola bilioni 2.5.

Mradi huo ni miongoni mwa miradi mikubwa ya kimkakati katika sekta ya madini nchini, ukiwa na matarajio ya kuibadili Tanzania kuwa kitovu muhimu cha uzalishaji wa madini ya nickel duniani.

Mkutano huu umefanyika katika wakati muafaka, ikizingatiwa kuwa Uamuzi wa Mwisho wa Uwekezaji (Final Investment Decision – FID) unatarajiwa kufanyika mwaka huu (2026).

Msajili wa Hazina alisisitiza kuwa Serikali itaendelea kusimamia kwa karibu utekelezaji wa mradi huo ili kuhakikisha unazingatia misingi ya uwazi, uwajibikaji na tija, huku ukitoa manufaa mapana kwa wananchi.

Bw. Mchechu alibainisha kuwa ushirikiano kati ya Serikali na wawekezaji unaonesha dhamira ya dhati ya kuendeleza rasilimali za nchi kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Kwa upande wake, Bw. Liddell alieleza kuridhishwa na maendeleo yaliyofikiwa katika hatua ya awali kabla ya FID, na kusisitiza dhamira ya kampuni kuendelea kushirikiana kwa karibu na Serikali ya Tanzania katika kuufanikisha mradi huo wa hadhi ya kimataifa.

Ilielezwa kuwa mradi huo unawakilisha fursa ya kipekee kwa Tanzania na kwa soko la kimataifa la nickel, hasa katika kipindi ambacho mahitaji ya madini hayo yanaongezeka kutokana na mabadiliko ya nishati na ukuaji wa teknolojia za kisasa.

Kwa mujibu wa upembuzi yakinifu uliokamilika Julai 2025, Kabanga ni miongoni mwa machimbo makubwa na yenye kiwango cha juu cha madini ya nickel sulfidi duniani yaliyo tayari kuendelezwa.

Mradi wa Kabanga unatarajiwa kuongeza thamani ya rasilimali za nickel kupitia matumizi ya teknolojia ya kisasa ya uchenjuaji, kukuza ajira kwa Watanzania, kuimarisha ujuzi wa ndani, na kuongeza mapato ya Serikali pamoja na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa kwa ujumla.

Aidha, utekelezaji wake utaimarisha mnyororo wa thamani katika sekta ya madini na kuongeza mchango wa sekta hiyo katika Pato la Taifa.

Kwa mujibu wa taarifa za kampuni, mikakati ya upatikanaji wa fedha inaendelea kwa mfumo wa njia nyingi (multi-track financing strategy), huku mazungumzo ya kina yakiendelea na wawekezaji wakubwa wa kimkakati, taasisi za kifedha na wanunuzi wa muda mrefu wa madini (off-takers).

Katika kuimarisha ushirikiano wa kimataifa, Desemba 8, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Tanzania, alifanya mazungumzo na Kaimu Balozi wa Marekani nchini Tanzania, Andrew Lentz, ambapo moja ya ajenda kuu ilikuwa kuharakisha ukamilishaji wa mikataba ya uwekezaji kwa Mradi wa Kabanga Nickel pamoja na miradi mingine ya kimkakati ya rasilimali asilia inayokaribia hatua ya ufadhili.

Kwa miezi ya karibuni, mikutano na maonesho ya uwekezaji (roadshows) imefanyika Tanzania, barani Ulaya, Japan, Afrika Kusini na Marekani, ikizihusisha taasisi za mikopo ya mauzo ya nje (Export Credit Agencies – ECAs) na benki za biashara.

Mradi wa Kabanga Nickel unaendelea kuonekana kuwa nguzo muhimu katika mkakati wa Tanzania wa kuongeza thamani ya rasilimali zake za madini, kuimarisha uchumi wa viwanda, na kujipanga vyema katika soko la kimataifa la madini muhimu kwa maendeleo ya teknolojia na nishati safi.


Mkuu wa Chuo cha VETA Shinyanga, Abraham Richard Mbughuni akizungumza na waandishi wa habari Machi 2, 2026 ofisini kwake kuhusu fursa zinazopatikana chuoni hapo ambazo zinaweza kuleta mabadiliko chanya kwa maisha ya vijana katika kupata ajira na kushiriki katika ujenzi wa uchumi wa nchi kupitia ujuzi watakaoupata.
Mkuu wa Chuo cha VETA Shinyanga, Abraham Richard Mbughuni akizungumza na waandishi wa habari.

Mkuu wa Chuo cha VETA Shinyanga, Abraham Richard Mbughuni akizungumza na waandishi wa habari Machi 2, 2026.


Na Kadama Malunde, Shinyanga


Chuo cha Ufundi Stadi Shinyanga (VETA) kimeendelea kujidhihirisha kuwa kitovu cha mapinduzi ya kiuchumi kwa vijana wa Mkoa wa Shinyanga kupitia upanuzi wa mafunzo ya ufundi stadi yanayolenga kuwawezesha kiujuzi, kuwaajiriwa na kujiajiri, hatua inayochochea ukuaji wa uchumi wa mkoa na taifa kwa ujumla.


Katika kuunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, chuo hicho kinaamini kuwa dunia ya sasa haihitaji vyeti pekee bali uwezo wa kufanya kazi kwa vitendo, kwa kuwa ujuzi ni mtaji, ujuzi ni ajira, ujuzi ni kujitegemea na ujuzi ni heshima.


Akizungumza na waandishi wa habari Machi 2, 2026 ofisini kwake kuhusu fursa zinazopatikana chuoni hapo ambazo zinaweza kuleta mabadiliko chanya kwa maisha ya vijana katika kupata ajira na kushiriki katika ujenzi wa uchumi wa nchi kupitia ujuzi watakaoupata, Mkuu wa Chuo hicho, Abraham Richard Mbughuni, amesema Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kuweka msisitizo mkubwa katika elimu ya ufundi stadi kama nguzo muhimu ya ajira na maendeleo ya taifa.

Mkuu wa Chuo cha VETA Shinyanga, Abraham Richard Mbughuni.


VETA NI MSINGI WA TANZANIA YA WATENDAJI


Amefafanua kuwa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) ni wakala wa Serikali ulioanzishwa kwa Sheria ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Sura ya 82, ukiwa na jukumu la kutoa, kugharamia na kuratibu mafunzo ya ufundi stadi nchini.


“Kwa lugha rahisi zaidi, VETA ndiyo inazalisha watu wanaojenga Tanzania kwa vitendo. Nyumba tunazoishi, barabara tunazopita, umeme tunaotumia, mashine viwandani, huduma za utalii, teknolojia za kilimo hadi matengenezo ya magari, yote yanategemea mafundi stadi,” amesisitiza.


Kwa mujibu wa Mkuu huyo wa Chuo, dira ya VETA ni “Tanzania yenye Mafundi Stadi Mahiri na wa Kutosha,” huku kaulimbiu ikiwa ni “Ufundi Stadi, Fursa Kama Zote, Kwa Watu Wote.”

UDAHILI WAONGEZEKA MARA MBILI


Katika kupanua fursa kwa vijana, VETA Shinyanga imeongeza kwa kiasi kikubwa idadi ya wanafunzi wanaodahiliwa kila mwaka. Kabla ya upanuzi wa miundombinu kupitia mradi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB) mwaka 2010, chuo kilikuwa na uwezo wa kudahili wanafunzi wapatao 400 wa kozi za muda mrefu na chini ya 1,200 wa kozi za muda mfupi kwa mwaka.


Kwa sasa, udahili umeongezeka hadi wanafunzi 545 wa kozi za muda mrefu na zaidi ya 3,000 wa kozi za muda mfupi kwa mwaka.


Ubora wa mafunzo yanayotolewa umevuka mipaka ya Tanzania, ambapo wanafunzi wa kozi za muda mfupi kutoka nchi za Afrika Mashariki na Kati wamekuwa wakijiunga na chuo hicho, na wengi wao kupata ajira ndani na nje ya nchi.


KOZI ZINAZOENDANA NA SOKO LA AJIRA


Mbughuni amesema chuo kimeboresha na kuanzisha kozi zinazoendana na mahitaji ya soko la ajira hususan katika sekta za madini, ujenzi na biashara ndogo ndogo zinazokua kwa kasi Shinyanga.

Kozi hizo ni pamoja na Umeme wa Majumbani na Viwandani, Uashi, Useremala, Ushonaji na Ubunifu wa Mavazi, Uchomeleaji na Uundaji Vyuma, Ufundi Mitambo, Ufundi Mitambo Mizito, Uhazili na TEHAMA, Ukataji na Ung’arishaji wa Madini Vito pamoja na Ufundi Bomba.

Aidha, kutokana na mwelekeo wa soko la ajira, chuo kimeanzisha kozi mpya za Ufundi Magari, Umeme wa Magari pamoja na Utengenezaji na Ukarabati wa Barabara.


MAFUNZO KWA MAKUNDI MAALUM NA MIRADI MIKUBWA


Chuo pia kimekuwa mstari wa mbele kutoa mafunzo kwa makundi maalum ikiwemo vijana wasio na ajira, wanawake na vikundi vya ujasiriamali.

Kupitia Programu ya Wanawake na Samia, washiriki 368 walipata mafunzo ya stadi mbalimbali, huku Mradi wa Bomba la Mafuta (EACOP) ukiwahusisha washiriki 20 (wanaume 16 na wanawake 4) waliopatiwa mafunzo kulingana na mahitaji ya mradi huo.

Lengo ni kuwawezesha kiujuzi na kiuchumi ili waweze kujiajiri au kuajiriwa na hivyo kuboresha maisha yao na kuchangia maendeleo ya taifa.


USHIRIKIANO NA VIWANDA NA URASIMISHAJI UJUZI


Katika kuhakikisha wahitimu wanakuwa tayari kwa soko la ajira, VETA Shinyanga imeimarisha ushirikiano na migodi, makampuni ya ujenzi, karakana binafsi na taasisi za umma kwa ajili ya mafunzo kwa vitendo (IPT) na mfumo wa Uanagenzi Pacha (DATS).

Pia chuo kinaendesha mpango wa Urasimishaji Ujuzi (Recognition of Prior Learning – RPL) kwa mafundi waliopata ujuzi nje ya mfumo rasmi. Mafundi hao hupimwa na kupewa vyeti vinavyotambulika kitaifa, hatua inayowawezesha kushiriki zabuni za Serikali na kupata ajira rasmi.


UNYUMBUFU NA UBORA WA MAFUNZO


Chuo kinapokea waombaji wote bila ubaguzi, wakiwemo wahitimu wa elimu ya juu wanaotaka kuongeza ujuzi wa vitendo (hands-on skills) ili kujiimarisha zaidi kiushindani katika soko la ajira.


Serikali imeendelea kuboresha karakana, madarasa na vifaa vya kisasa vya kufundishia, huku watumishi wakipewa mafunzo ya kuongeza umahiri ili kuendana na mabadiliko ya teknolojia na mahitaji ya soko.


UJUMBE MZITO KWA VIJANA


Katika ujumbe wake kwa vijana, Mbughuni amesisitiza kuwa dunia ya leo haihitaji vyeti pekee bali uwezo wa kufanya kazi kwa vitendo.


“Ujuzi ni mtaji, ujuzi ni ajira, ujuzi ni kujitegemea na ujuzi ni heshima. Hivyo ninawahamasisha vijana wote kuja VETA Shinyanga kujifunza stadi mbalimbali ili wajiajiri na kuajiri wengine”, amesema.


VETA – INJINI YA AJIRA NA UCHUMI SHINDANI


Mkuu huyo wa Chuo amesema kupitia uwekezaji wa Serikali ya Awamu ya Sita, VETA imekuwa injini ya kuzalisha ajira na uchumi shindani.


Ameomba wanahabari kuwa mabalozi wa kuelimisha jamii kuhusu fursa zinazotolewa na chuo hicho ili kila kijana ajue kuwa mustakabali wake uko mikononi mwake.


“Tunatambua kuwa Ufundi Stadi, Fursa Kama Zote, Kwa Watu Wote. VETA Shinyanga, Kazi Mkononi,” amesema Mbughuni.

Top News