Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya eneo la Ngorongoro Abdul-Razaq Badru ameuambia mkutano wa 48 wa kamati ya Urithi wa Dunia kuwa Ngorongoro ni sehemu pekee ambayo binadamu duniani kote wanaweza kupata ushahidi sahihi wa chimbuko la asili ya binadamu.

Akizungumza mjini Busan,Jamhuri ya Korea wakati akiongoza Mkutano wa pembeni (Side event) ulioandaliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa lengo la kupata uelewa wa pamoja kuhusu hali ya uhifadhi wa eneo la  Hifadhi ya Ngorongoro ambayo ni eneo la Urithi wa Dunia, Badru amesema Ngorongoro ina ushahidi uliohifadhiwa wa nyayo za binadamu na masalia ya kale katika eneo la Laetoli na Olduvai zinazothibitisha suala hilo.

“Ngorongoro si tu eneo la utalii bali pia ni mahali ambapo historia ya binadamu wote kisayansi ilianzia”, alisema kamishna Badru.

Katika kikao hicho ameeleza kuwa kila nyayo iliyohifadhiwa ndani ya hifadhi ya Ngorongoro inawakumbusha kurudi nyumbani kuona historia hiyo.

Badru amefafanua  kuwa Ngorongoro ni sehemu ambayo binadamu alianzia kutumia zana mbalimbali za mawe kama teknolojia ya awali ya shughuli za kibinadamu na ndipo alipoanza kufanya harakati za kimaisha.

Mkutano wa kamati ya Urithi wa Dunia una lengo la kufanya maamuzi kuhusu maeneo mapya yanayopendekezwa kuingizwa kwenye Orodha ya Urithi wa Dunia na kuimarisha juhudi za pamoja za kulinda, kuhifadhi, na kusimamia kwa uendelevu maeneo yenye thamani kubwa ya kiutamaduni na asili duniani.




 ■ Waziri Mavunde ataka mnyororo wote wa utoroshaji wa madini hayo udhibitiwe,

■ Asikitishwa na upotevu wa mapato ya Serikali yatokanayo na vitendo hivyo,

■ Aelekeza wahusika wote wafutiwe leseni na kutoruhusiwa tena kufanya biashara ya madini,

■ Atoa rai kwa wananchi kufanya biashara ya madini kupitia mfumo rasmi


📍Dar es Salaam,

Kufuatia kuimarishwa kwa mfumo wa udhibiti wa biashara haramu ya madini unaofanywa na Wizara ya Madini kupitia Kikosi Kazi (Taskforce), madini aina ya dhahabu Gramu 4,402.20 yenye thamani ya 1,238,458,594.42 yamekatwa yakitoroshwa.

Hayo yamesemwa leo tarehe 27 Julai, 2026 na Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde (Mb) Jijini Dar es Salaam alipokuwa akizungumza na vyombo vya habari.

"Serikali kupitia Wizara ya Madini iliunda Kikosi kazi ambacho kinahusisha vyombo vya dola ili kudhibiti biashara haramu ya madini na utoroshaji. Hii ni sehemu tu ya kazi ambazo zimeendelea kufanywa na Kikosi kazi hicho katika kuimarisha mfumo wa ufanyaji biashara ya madini"

"Ndugu zangu, dhahabu hii yenye zaidi ya thamani ya bilioni 1.2 haikupitia katika mfumo rasmi wa ufanyaji biashara ya madini na hivyo kupelekea Serikali kukosa mapato ambayo yangeisaidia kuimarisha utoaji wa huduma mbalimbali kwa wananchi" Alisisitiza Mhe. Mavunde.

Aidha, Waziri Mavunde alibainisha kuwa dhahabu hiyo iliyokamatwa imetaifishwa kwa mujibu wa taratibu za Sheria na imehifadhiwa Benki Kuu ya Tanzania.

Vilevile, Mheshimiwa Mavunde amekielekeza Kikosi Kazi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya dola kumhoji vizuri mtuhumiwa aliyekamatwa na dhahabu hizo kufahamu alikotoka na alikuwa anapeleka wapi, ili kuweza kutibu kabisa mzizi wa vitendo hivyo na kuvunja mnyororo wa wote wa utoroshaji.

Mhe. Mavunde alisisitiza kuwa, iwapo mtuhumiwa aliyekamatwa alikuwa na leseni ya ufanyaji biashara ya madini kufutiwa leseni hiyo mara moja na kuingizwa kwenye orodha maalum ya wenye makosa (blacklisted) ili asiruhusiwe tena kufanya biashara ya madini nchini.

Katika hatua nyingine, Waziri Mavunde alitoa rai kwa wananchi wote kuzingatia na kufuata sheria na mifumo ya ufanyaji biashara ya madini ambayo tumejiwekea kupitia masoko ya madini na vituo vya ununuzi ambavyo vimesambaa Nchi nzima.





Kampuni ya huduma za fedha kidijitali Mixx imewataka Watanzania kuendelea kutumia huduma zake huku ikitangaza kuwa droo ya mwisho ya kampeni ya "Ikiingia Tu Goli" itafanyika wiki ijayo, ambapo mshindi mmoja atajishindia Shilingi milioni 50.

Akizungumza wakati wa kukabidhi zawadi kwa washindi wa droo ya tisa ya kampeni hiyo inayofanyika kwa ushirikiano na Hisense, Mkuu wa Idara ya Makampuni na Washirika - Mixx, Bw. Justine Lawena, alisema kampeni hiyo imeendelea kuwahamasisha Watanzania kutumia huduma za kifedha kidijitali huku ikiwazawadia fedha taslimu na vifaa mbalimbali.

Katika droo hiyo, washindi 10 walipatikana, ambapo saba walijishindia Shilingi milioni moja kila mmoja, huku watatu wakijishindia vifaa vya Hisense. Lawena alisema hadi sasa kampeni hiyo imewazawadia zaidi ya Watanzania 90 tangu ilipoanza.

"Fainali za Kombe la Dunia zimekwisha, lakini fainali ya kampeni yetu ndiyo inafuata wiki ijayo. Hapo ndipo tutampata mshindi wa Shilingi milioni 50. Bado kila Mtanzania ana nafasi ya kushinda kwa kutumia Mixx Super App," alisema Lawena.

Alisema ili kushiriki droo ya mwisho, mteja anatakiwa kutumia Mixx Super App kufanya miamala kama kutuma na kupokea fedha, kulipa bili na kufanya malipo ya Serikali.

Lawena aliwataka wateja kuwa makini wanapopigiwa simu kutoka namba 100, akieleza kuwa hiyo ndiyo namba rasmi ya kuwataarifu washindi.

"Tunawakumbusha wateja kupokea simu kutoka namba 100. Usipoipokea unaweza kupoteza fursa ya kuthibitisha ushindi wako. Bado una nafasi ya kushinda kwa kuendelea kutumia Mixx Super App," alisema.

Mmoja wa washindi wa Shilingi milioni moja, Bw. David Kisusi, alisema ushindi huo umempa motisha zaidi kuendelea kutumia Mixx kutokana na urahisi na usalama wa huduma zake.

"Nimekuwa nikitumia Mixx kwa shughuli zangu za kila siku na ninaweza kulipia bili mbalimbali kwa urahisi kupitia simu yangu. Kinachonivutia zaidi ni usalama wa huduma hizi, kwani hata muamala unapokwenda kimakosa, kuna msaada wa haraka wa kuuzuia au kuurejesha," alisema Kisusi.

Kampeni ya "Ikiingia Tu Goli", inayofanyika kwa ushirikiano kati ya Mixx na Hisense, inalenga kuhamasisha matumizi ya huduma za kifedha kidijitali nchini huku mshindi wa mwisho akitarajiwa kujishindia Shilingi milioni 50.
Mkuu wa Idara ya Makampuni na Washirika wa Mixx, Justine Lawena (kushoto), akimkabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya Shilingi milioni moja kwa Bw. David Kisusi, mmoja wa washindi wa kampeni ya "Ikiingia tu Goli", wakati wa hafla ya kukabidhi zawadi iliyofanyika katika ofisi za kampuni jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki. Kampeni hiyo, inayoendeshwa kwa ushirikiano na Hisense, imefanikiwa kuwazawadia zaidi ya Watanzania 90 fedha taslimu na vifaa vya kielektroniki kwa kutumia huduma za kifedha kidijitali za Mixx, huku mshindi wa zawadi kuu ya Shilingi milioni 50 akitarajiwa kutangazwa katika droo ya mwisho wiki ijayo.




 Kampuni ya mawasiliano ya Yas Tanzania imezindua rasmi msimu wa sita wa mbio za Yas Zanzibar International Marathon 2026, ikiahidi kuendelea kuwekeza katika michezo, afya ya jamii na utalii wa michezo huku usajili wa washiriki ukifanyika kidijitali kupitia Mixx.

Yas ni mdhamini wa mashindano hayo kwa mwaka wa tano mfululizo na kwa mwaka huu mashindano yanatarajia kuvutia zaidi ya wakimbiaji elfu kumi (10,000) wa ndani nan je ya Tanzania, hatua inayolenga kuendelea kuitangaza Zanzibar kama moja ya nchi Kinara kwa utalii na michezo barani Afrika.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo Zanzibar, Dkt. Riziki Pembe Juma, alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na sekta binafsi katika kuendeleza matukio ya michezo yanayochochea uchumi, kukuza utalii na kuhamasisha wananchi kuishi maisha yenye afya.

"Yas Zanzibar International Marathon imeendelea kuwa zaidi ya mashindano ya riadha. Ni jukwaa linaloitangaza Zanzibar duniani, linakuza utalii wa michezo, linaibua vipaji na kuwahamasisha wananchi kuzingatia mazoezi kama sehemu ya maisha yenye afya. Serikali itaendelea kuunga mkono juhudi za wadau wanaowekeza katika maendeleo ya michezo na afya ya jamii," alisema Dkt. Pembe.

Kwa upande wake, Afisa Mkuu wa Fedha wa Yas Tanzania, Innocent Rwetabura, alisema kampuni hiyo inaendelea kutumia michezo kama njia ya kuunganisha jamii, kuhamasisha mtindo wa maisha wenye afya na kuchochea ukuaji wa utalii wa michezo.

Alisema ongezeko la washiriki wa marathon hiyo kila mwaka linaonyesha mwamko unaoongezeka wa Watanzania kuhusu umuhimu wa mazoezi, hasa katika kipindi ambacho taifa linaendelea kukabiliana na magonjwa yasiyoambukiza.

"Yas Zanzibar International Marathon imekuwa jukwaa muhimu linalowaunganisha watu kutoka ndani na nje ya Tanzania, kukuza vipaji vya vijana na kuitangaza Zanzibar kama kitovu cha utalii wa michezo. Kadri idadi ya washiriki na wageni inavyoongezeka, ndivyo fursa zinavyoongezeka kwa sekta ya utalii, wafanyabiashara na uchumi wa Zanzibar kwa ujumla," alisema Rwetabura.

Aliongeza kuwa usajili na malipo yote ya washiriki yatafanyika kidijitali kupitia Mixx, hatua inayolenga kurahisisha huduma na kuwapa washiriki uzoefu wa kisasa wenye viwango vya kimataifa.

Mbali na udhamini wa mbio hizo, alisema Yas inaendelea kuwekeza katika kuboresha miundombinu ya mawasiliano Zanzibar kupitia huduma za Fiber pamoja na mtandao wa 4G na 5G ili kuendana na mahitaji ya ukuaji wa uchumi wa kidijitali.

Marathon ya mwaka huu itafanyika chini ya kaulimbiu ya "Kasi Swadakta kwa Viwango", huku waandaaji wakiwahimiza Watanzania na washiriki kutoka mataifa mbalimbali kujisajili mapema kushiriki tukio hilo la kimataifa linalotarajiwa kuvutia maelfu ya wakimbiaji na watalii visiwani Zanzibar.

aziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo Zanzibar, Dkt. Riziki Pembe Juma (katikati), akifurahia jambo na wadhamini na wadau wa Yas Zanzibar International Marathon mara baada ya uzinduzi rasmi wa msimu wa sita wa mbio hizo kwa mwaka 2026, katika hafla iliyofanyika jana visiwani Zanzibar. Wengine pichani ni Afisa Mkuu wa Fedha wa Yas Tanzania, CPA Innocent Rwetabura (kushoto), Mkurugenzi wa Uendeshaji wa Mixx, Bw. Arnold Ngarashi (kulia), Mjumbe wa Bodi ya Zanzibar Marathon, Bw. Hassan Zanga (wa pili kulia), na Mkurugenzi wa Taasisi ya Mwanamke Initiative Foundation, Sabra Ali Mohamed (wa pili kushoto).

Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo Zanzibar, Dkt. Riziki Pembe Juma (katikati), akifurahia jambo wakati wa uzinduzi wa mbio za Yas Zanzibar International Marathon mara baada ya uzinduzi rasmi wa msimu wa sita wa mbio hizo kwa mwaka 2026, katika hafla iliyofanyika jana visiwani Zanzibar. Wengine pichani ni Afisa Mkuu wa Fedha wa Yas Tanzania, CPA Innocent Rwetabura (kushoto) na kulia ni Bw. Said Kassim Marin - Katibu Mtendaji wa Baraza la Michezo Zanzibar


Tanzania imepiga hatua nyingine kimataifa baada ya Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC) kuorodhesha hatifungani yake ya kwanza ya kimataifa kwa Shilingi ya Tanzania katika Soko la Hisa la London (LSE). 

Hatifungani hiyo, yenye thamani ya Dola za Marekani milioni 100 (Shilingi bilioni 262.5), itaipatia Benki ya NMB ikiwa ni fedha za muda mrefu kwa ajili ya kupanua mikopo kwa biashara ndogo na za kati, huku asilimia 20 - sawa na Shilingi bilioni 52.5 - ikitengwa mahsusi kwa wafanyabiashara wanawake.

Akizungumza baada ya kupiga kengele ya uzinduzi, Mkurugenzi Mkuu wa NMB, Ruth Zaipuna, alisema fedha hizo zitaongeza uwezo wa benki kutoa mikopo ya muda mrefu, jambo litakalochochea ukuaji wa sekta binafsi na ajira. Naye Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar, alisema hatua hiyo inaonesha imani ya kimataifa kwa uchumi wa Tanzania na inaunga mkono Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Fedha hizi, zinazotolewa kwa Shilingi badala ya fedha za kigeni, zinawawezesha wafanyabiashara kupata mtaji bila hatari ya mabadiliko ya thamani ya fedha. Hii ni mara ya pili NMB kufaidika na soko la London - mwaka 2023 benki ilikusanya zaidi ya Shilingi bilioni 400 kupitia hatifungani ya kijamii. 






Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, leo ameongoza zaidi ya washiriki 13,000 katika mbio za NBC Dodoma Marathon 2026 zilizofanyika katika Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma, huku akiipongeza Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) kwa kufanikisha ukusanyaji wa shilingi bilioni 1 zitakazotumika kuokoa maisha ya maelfu ya Watanzania kupitia miradi ya afya ya mama na mtoto.

Fedha hizo zitasaidia utekelezaji wa maeneo matatu muhimu ya kijamii ambayo ni kupunguza vifo vya akina mama na watoto wakati wa kujifungua, kugharamia upasuaji wa watoto wenye matatizo ya moyo, pamoja na kuimarisha huduma za upandikizaji wa uloto kwa watoto wanaoishi na ugonjwa wa selimundu (Sickle Cell).

Mbio hizo, ambazo zimeendelea kujijengea hadhi kama moja ya matukio makubwa zaidi ya michezo nchini, zilihusisha washiriki kutoka Tanzania na mataifa mbalimbali, huku zikishuhudia ushindani mkubwa kati ya wanariadha wa Tanzania na Kenya katika mbio za kilomita 21 na 42. Dkt. Nchemba, pamoja na viongozi mbalimbali wa Serikali, taasisi na sekta binafsi, walishiriki mbio za kilomita tano (5) kuhamasisha mazoezi na maisha yenye afya.

Akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi zawadi kwa washindi na wadau wa mbio hizo, Dkt. Nchemba alisema mafanikio ya NBC Dodoma Marathon yanaonesha jinsi ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi unavyoweza kuleta matokeo yenye manufaa makubwa kwa jamii.

Alisema ongezeko la washiriki kutoka 1,500 mwaka 2020 hadi zaidi ya 13,000 mwaka 2026 ni ushahidi wa mwamko mkubwa wa Watanzania katika kushiriki michezo, kuzingatia afya zao na kuunga mkono shughuli za maendeleo kupitia michezo.

"NBC Dodoma Marathon imekuwa zaidi ya mashindano ya riadha. Leo ni jukwaa linalounganisha Watanzania na marafiki kutoka mataifa mbalimbali kwa lengo la kufanya jambo kubwa zaidi—kuokoa maisha. Nawahimiza Watanzania kujenga utamaduni wa kufanya mazoezi mara kwa mara ili kujikinga dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza kama vile kisukari, shinikizo la damu, magonjwa ya moyo na figo," alisema Dkt. Nchemba.

Aidha alisema Serikali itaendelea kuboresha miundombinu ya barabara katika Jiji la Dodoma kwa kupanua na kuboresha barabara muhimu, hatua itakayorahisisha shughuli za usafirishaji na wakati huo huo kuongeza usalama wa washiriki wa mbio hizo katika miaka ijayo.

Waziri Mkuu pia aliutaka uongozi wa Mkoa wa Dodoma kuendelea kuziunga mkono mbio hizo kutokana na mchango wake mkubwa katika kukuza uchumi wa jiji hilo kupitia ongezeko la wageni, shughuli za utalii wa ndani, biashara za hoteli, migahawa, usafiri na huduma nyingine zinazochochewa na tukio hilo.

Awali, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Bi. Rosemary Senyamule, alisema NBC Dodoma Marathon imeendelea kuwa kichocheo muhimu cha uchumi wa mkoa huo kwa kuongeza mzunguko wa fedha na kutoa fursa kwa wafanyabiashara wadogo na wakubwa kila mwaka.

Aliishukuru Benki ya NBC kwa kuendelea kuwa mshirika mkubwa wa maendeleo ya Mkoa wa Dodoma kupitia uwekezaji wake katika afya, michezo na maendeleo ya jamii.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC, Bw. Theobald Sabi, alisema mafanikio ya mbio hizo yanaakisi dhamira ya benki hiyo ya kuendelea kutumia biashara kama chachu ya kuleta maendeleo ya kijamii.

Alisema kati ya fedha zilizokusanywa, shilingi milioni 600 zimeelekezwa moja kwa moja katika utekelezaji wa malengo makuu ya NBC Dodoma Marathon kupitia taasisi tatu zinazotoa huduma muhimu za afya nchini.

Katika hafla hiyo, Dkt. Nchemba na Bw. Sabi walikabidhi hundi za misaada ambapo: Shilingi milioni 200 zilikabidhiwa Taasisi ya Benjamin Mkapa kwa ajili ya kupanua programu ya ufadhili wa wakunga ili kuboresha huduma za afya ya uzazi, Shilingi milioni 200 zilikabidhiwa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) kwa ajili ya kugharamia upasuaji wa watoto wenye matatizo ya moyo na Shilingi milioni 200 zilikabidhiwa Hospitali ya Benjamin Mkapa kusaidia huduma za upandikizaji wa uloto kwa watoto wenye ugonjwa wa selimundu.

"Mafanikio haya yanatokana na dhamira yetu ya kuhakikisha mafanikio ya biashara yanaenda sambamba na ustawi wa jamii. Tunawashukuru washiriki wote, wadhamini na wadau mbalimbali waliochangia kufanikisha NBC Dodoma Marathon 2026. Ushirikiano huu umewezesha kuokoa maisha ya Watanzania wengi," alisema Bw. Sabi.

Alitoa shukrani maalumu kwa wadhamini wakuu wa mbio hizo akiwemo Sanlam Allianz, GSM Group, Vodacom Tanzania, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) pamoja na wadau wengine waliochangia mafanikio ya tukio hilo.

Katika mbio za kilomita 42 (Full Marathon) kwa upande wa wanaume, mwanariadha kutoka Kenya Edwin Koech aliibuka mshindi wa kwanza kwa kutumia muda wa saa 2:05:12, akifuatiwa na Vitalis Kibiwott aliyemaliza kwa saa 2:12:18.

Kwa upande wa wanawake, Agnes Ngolo wa Kenya alitwaa ushindi kwa kutumia muda wa saa 2:32:36, huku Jacinta Chepkoech, pia kutoka Kenya, akimaliza wa pili kwa muda wa saa 2:33:26.

Washindi wa nafasi ya kwanza hadi ya kumi walizawadiwa fedha taslimu, ambapo washindi wa kwanza wa mbio za kilomita 42 kwa wanaume na wanawake kila mmoja alijishindia Tsh milioni 11.5.

Katika mbio za kilomita 21 (Half Marathon) kwa wanaume, Bernard Geay wa Tanzania aliibuka mshindi wa kwanza kwa muda wa saa 1:02:46, akifuatiwa na Simon Kelenzoke wa Kenya (1:02:57), huku nafasi ya tatu ikichukuliwa na Michael Geay wa Tanzania kwa muda wa 1:02:59.

Kwa upande wa wanawake, Magdalena Shauri wa Tanzania aliibuka mshindi wa kwanza kwa muda wa 1:08:59, akifuatiwa na Doreen Chetzop wa Kenya aliyemaliza kwa muda wa 1:10:36.

Washindi wa kwanza wa mbio za kilomita 21 kwa wanaume na wanawake walijishindia Tsh milioni 5.5, huku washindi wa pili wakiondoka na Tsh milioni 2.5.

NBC Dodoma Marathon imeendelea kuthibitisha kuwa si tu tamasha kubwa la michezo nchini, bali pia ni jukwaa la kuhamasisha afya, kuunganisha jamii, kukuza uchumi wa Jiji la Dodoma na kuchangia moja kwa moja kuboresha huduma muhimu za afya kwa Watanzania.


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, (katikati) akimkabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya Tsh milioni 200 kwa muwakilishi wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) (wanne kushoto) iliyotolewa na Benki ya NBC kwa ajili ya kugharamia upasuaji wa watoto wenye matatizo ya moyo kupitia mbio za NBC Dodoma Marathon zilizofanyika leo kwenye Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma. Wanaoshuhudia ni pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Bi. Rosemary Senyamule (wa tatu kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC Bw Theobald Sabi (wa nne kulia), Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya benki ya NBC , Dkt. Elirehema Doriye (wa pili kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa SanlamAllianz, wadhamini wakuu wa mbio hizo, Bw Julius Magabe (kushoto) na viongozi wengine kutoka serikalini na wadau wa mbio hizo.




Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, (katikati) akimkabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya Tsh milioni 200 kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Benjamin Mkapa, Profesa Abel Makubi (wa tatu kushoto) iliyotolewa na Benki ya NBC kwa ajili ya kusaidia huduma za upandikizaji wa uloto kwa watoto wenye ugonjwa wa selimundu (sicke cell)kupitia mbio za NBC Dodoma Marathon zilizofanyika leo kwenye Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma. Wanaoshuhudia ni pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Bi. Rosemary Senyamule (wa pili kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC Bw Theobald Sabi (wa pili kulia), Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya benki hiyo, Dkt. Elirehema Doriye (kushoto) na viongozi wengine kutoka serikalini na wadau wa mbio hizo.


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, (katikati) akimkabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya Tsh milioni 200 kwa muwakilishi wa Taasisi ya Benjamin Mkapa Foundation (wanne kushoto) iliyotolewa na Benki ya NBC kwa ajili ya kwa ajili ya kupanua programu ya ufadhili wa wakunga ili kuboresha huduma za afya ya uzazi kupitia mbio za NBC Dodoma Marathon zilizofanyika leo kwenye Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma. Wanaoshuhudia ni pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Bi. Rosemary Senyamule (wa tatu kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC Bw Theobald Sabi (wa nne kulia), Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya benki ya NBC , Dkt. Elirehema Doriye (wa pili kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa SanlamAllianz, wadhamini wakuu wa mbio hizo, Bw Julius Magabe (kushoto) na viongozi wengine kutoka serikalini na wadau wa mbio hizo.


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, (wa tatu kushoto) akikabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya sh mil 5.5 kwa mwanariadha kutoka Tanzania, Magdalena Shauri alieibuka mshindi wa kwanza (kwa upande wa wanawake) wa mbio za km 21 za NBC Dodoma Marathon, zilizofanyika leo kwenye Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma. Wanaoshuhudia ni pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC Bw Theobald Sabi (wa pili kulia) na viongozi wengine kutoka serikalini na wadau wa mbio hizo.



Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, (kushoto) akikabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya sh mil 11.5 kwa mwanariadha kutoka Kenya, Edwin Koech alieibuka mshindi wa kwanza (kwa upande wa wanaume) wa mbio za km 42 za NBC Dodoma Marathon, zilizofanyika leo kwenye Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma. Wanaoshuhudia ni pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC Bw Theobald Sabi (kulia)

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ametembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa Uwanja wa Arusha, utakaotumika katika michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika mwaka 2027 (AFCON 2027), unaojengwa Jijini Arusha.

 Makamu wa Rais amepongeza maendeleo ya ujenzi wa uwanja huo, ambapo amesema ni faraja kuona ahadi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyoitoa ili kuvutia michuano hiyo kufanyika nchini Tanzania, inatakelezwa kikamilifu. Amemshukuru Mhe. Rais kwa kuendelea kutoa fedha ili kuhakikisha uwanja huo unakamilika kwa wakati.

Aidha, Makamu wa Rais ameishukuru Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo pamoja na mkoa wa Arusha, Wakandarasi na Mshauri Elekezi kwa kazi kubwa waliyofanya katika Uwanja huo.

 Makamu wa Rais amewataka Viongozi wa Wizara pamoja na Mkoa wa Arusha kusimamia vema agizo la Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan la kuhakikisha barabara zinazotumika katika kufika uwanjani hapo zinakamilika kwa wakati.

Awali Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. Amos Makala, amemueleza Makamu wa Rais, maendeleo ya ujenzi wa uwanja huo ambao umefikia asilimia 88, ukitarajiwa kukamilika ifikapo mwishoni mwa mwezi Agosti, 2026.

 Uwanja wa Arusha, utakapokamilika, mbali na michezo, unatarajiwa kuwa kivutio cha utalii ukiwa umebeba alama ya Mlima Kilimanjaro, Madini ya Tanzanite na Bendera ya Taifa.












 



SAME.

MKUU wa Wilaya ya Same, Kasilda Mgeni, amewaonya wananchi wanaojihusisha na uchimbaji haramu wa madini ndani ya mita 60 kutoka kwenye vyanzo vya maji, akisisitiza kuwa hakuna mtu au mwekezaji mwenye kibali cha kufanya shughuli za uchimbaji huo.

Amesema Serikali ya wilaya imeanza kuwachukulia hatua za kisheria, kwa lengo la kulinda vyanzo vya maji, mazingira na maslahi ya wananchi.

Hatua hiyo imekuja jana baada ya Kasilda, akiambatana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya wilaya pamoja na wataalamu kutoka Ofisi ya Madini na Bonde la Mto Pangani, kutembelea baadhi ya maeneo yanayofanyika uchimbaji haramu wa madini na kujionea uharibifu mkubwa wa mazingira katika vyanzo vya maji vilivyopo Kata ya Mhezi.

Kasilda alisema ni kosa kisheria kuanza shughuli za uchimbaji wa madini bila kuwa na leseni au kibali kutoka Ofisi ya Madini, pamoja na kufanya shughuli yoyote ndani ya umbali wa mita 60 kutoka kwenye vyanzo vya maji bila kibali kutoka Bonde la Mto Pangani.

Alibainisha kuwa serikali imeanza kuwachukulia hatua wahusika wote ili kunusuru uharibifu wa mazingira na athari zinazoweza kujitokeza kutokana na shughuli hizo haramu.

"Ni kosa kisheria kuanza kuchimba madini bila kuwa na leseni au kibali husika kutoka Ofisi ya Madini na kufanya shughuli yoyote ndani ya mita 60 kutoka kwenye chanzo cha maji bila kibali kutoka Ofisi za Bonde. Wote wanaohusika tumeanza kuwashughulikia mara moja kwa lengo la kunusuru uharibifu na athari kubwa zinazoweza kutokea kutokana na uchimbaji huo haramu," alisema Kasilda.








NA DENIS MLOWE, IRINGA


MBUNGE wa Jimbo la Iringa Mjini, Fadhili Ngajilo, ametoa wito kwa wananchi, wadau wa michezo, wafanyabiashara na wazawa wa Iringa waliopo ndani na nje ya mkoa kushirikiana kuanzisha mfuko maalumu utakaowezesha kurejeshwa kwa timu ya Ligi Kuu Tanzania Bara itakayoiwakilisha Iringa.

Ngajilo alitoa kauli hiyo wakati wa kukabidhi vifaa vya michezo kwa timu 16 zilizofuzu hatua ya 16 bora ya mashindano ya Ngajilo Super League 2026 yaliyofanyika katika Uwanja wa Samora mjini Iringa.

Alisema baada ya miaka 15 tangu kuanzishwa kwa mashindano hayo mwaka 2010, sasa umefika wakati wa kuyatumia kama msingi wa kuimarisha maendeleo ya soka na kufanikisha ndoto ya mkoa kuwa na timu ya Ligi Kuu.

"Majadiliano ya kuwa na timu ya Ligi Kuu yamekuwa mengi sasa umefika wakati wa kugeuza maneno kuwa vitendo kwani Iringa inahitaji timu itakayobeba heshima na kuitangaza mkoa wetu nchini," alisema Ngajilo.

Alisisitiza kuwa timu hiyo haitakuwa mali ya wilaya au jimbo moja bali ya Mkoa mzima wa Iringa, akiwataka wananchi wa Kilolo, Mufindi, Isimani, Kalenga, Iringa Mjini pamoja na wazawa wanaoishi Dar es Salaam, Dodoma, Mbeya, Njombe, Morogoro na maeneo mengine kushiriki katika ujenzi wa timu hiyo.

Ngajilo alisema changamoto kubwa si kununua timu bali ni kuimudu kifedha, hivyo akashauri kuanzishwa mfumo wa kisasa wa usajili wa wanachama na uchangiaji wa fedha kwa njia za kidijitali ili kuhakikisha timu inakuwa na chanzo cha mapato cha uhakika.

Alieleza kuwa hata michango midogo ya shilingi 1,000 kwa mwezi kutoka kwa maelfu ya wananchi inaweza kuwa msingi wa kuiendesha timu kwa ufanisi, huku akipendekeza kuundwa kwa kamati maalumu ya fedha itakayosimamia ukusanyaji na matumizi ya michango hiyo.

Ngajilo aliwataka viongozi wa soka kuanza kujenga mifumo imara ya kifedha kabla ya kuanza mchakato wa kununua timu, akisema ni muhimu kuhakikisha kuna fedha za kutosha kwa ajili ya mishahara ya wachezaji, safari, malazi, vifaa na mahitaji mengine ya uendeshaji.

Aidha aliwahimiza wadau wengine kujitokeza kuunga mkono Ngajilo Super League ili maendeleo ya soka yasitegemee mfadhili mmoja pekee, huku akiwapongeza viongozi wa Chama cha Soka Wilaya ya Iringa (IDFA) kwa usimamizi mzuri wa mashindano hayo.

Katibu wa IDFA, Yahaya Mpelembwa, alimpongeza Mbunge Ngajilo kwa kuendelea kuwekeza katika maendeleo ya soka kwa miaka mingi na kusema mchango wake umeiwezesha ligi hiyo kukua kutoka ngazi ya Manispaa hadi kushirikisha timu kutoka majimbo ya Iringa Mjini, Isimani na Kalenga.

Alisema timu 16 zilizofuzu zimepatikana baada ya ushindani mkali wa ligi na sasa zitacheza hatua ya mtoano (knockout) hadi kupatikana bingwa atakayewakilisha Wilaya ya Iringa katika mashindano ya ngazi ya mkoa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa IDFA, Joel Musiba, alisema Ngajilo ameendelea kuwa mdhamini mkuu wa ligi hiyo kwa misimu zaidi ya mitano bila ubaguzi, jambo lililochochea ukuaji wa soka la wilaya.

Musiba alisema chama hicho hakifanyi siasa bali kina wajibu wa kushirikiana na wadau wote wanaosaidia maendeleo ya michezo, akiwataka viongozi wa timu kuhakikisha wanathamini wadhamini kwa kuvaa jezi zenye nembo ya mdhamini rasmi wa mashindano.

Pia alimuomba Mbunge huyo kuendelea kuisaidia timu itakayotwaa ubingwa wa Ngajilo Super League katika safari yake ya kushiriki mashindano ya ngazi ya mkoa ili kuongeza nafasi ya Iringa kupata timu itakayopanda madaraja hadi kufikia Ligi Kuu Tanzania Bara.

Mashindano ya Ngajilo Super League yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kuibua vipaji vya soka na kuimarisha ushindani wa timu za wilaya, huku wadau wakiamini kuwa yanaweza kuwa nguzo ya kurejesha hadhi ya soka la Mkoa wa Iringa.





Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Cambridge cha Uingereza, wameaanzisha utafiti wa vinasaba unaolenga kuboresha matibabu ya saratani ya tezi kwa watoto nchini Tanzania na ukanda wa Afrika.

Akieleza kuhusu utafiti huo, Dkt. Advera Ngaiza, Bingwa wa Uchunguzi wa Magonjwa ya Saratani amesema mradi huo utahusisha uchukuaji wa sampuli za vinasaba na tishu kutoka kwa watoto wenye saratani ya tezi nchini Tanzania. 

Amesema sampuli hizo zitachakatwa katika Maabara Kuu ya MNH, huku uchunguzi wa kina wa kisayansi ukifanyika ili kuelewa kwa nini matibabu ya sasa hayatoi matokeo mazuri kwa watoto wa Kiafrika. 

"Lengo letu ni kugundua dawa salama, sahihi na yenye ufanisi mkubwa zaidi itakayosaidia kutibu saratani ya tezi kwa watoto katika ukanda wa Afrika."

Hatua hii inakuja baada ya kubainika kuwa mifumo mingi ya sasa ya matibabu haitoi matokeo yanayotarajiwa kwa watoto wa ukanda huu wa afrika ikilinganishwa na maeneo mengine duniani. 

Kupitia utafiti huu, watafiti wanatarajia kuweka msingi wa maendeleo ya tiba zinazozingatia tofauti za vinasaba, hatua ambayo inaweza kuleta mapinduzi makubwa katika huduma za matibabu ya saratani kwa watoto barani Afrika.






 


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo Julai 25, 2026 ameongoza Maadhimisho ya Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa yaliyofanyika katika Uwanja wa Mashujaa, Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.

Rais Samia aliwasili katika viwanja vya maadhimisho na kupokelewa kwa heshima rasmi za kijeshi, kabla ya kupokea heshima ya wimbo wa Taifa la Tanzania na wimbo wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Katika kilele cha maadhimisho hayo, Rais Samia aliweka mkuki na ngao kwenye Mnara wa Mashujaa ikiwa ni ishara ya kutoa heshima kwa mashujaa waliojitolea kwa ujasiri na uzalendo kwa ajili ya Taifa.

Maadhimisho hayo yalihudhuriwa na viongozi wa Serikali, vyombo vya ulinzi na usalama, wanajeshi wastaafu, viongozi wa dini pamoja na wananchi na wageni mbalimbali.

Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa huadhimishwa tarehe 25 Julai ya kila mwaka kwa lengo la kuwakumbuka na kuwaheshimu mashujaa waliopigania uhuru wa nchi na wale waliojitolea kulinda amani, usalama na maslahi ya Taifa.

Top News