Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo,akizungumza Julai 31, 2026 Jijini Dar es Salaam wakati akifungua Kikao cha Kamati Elekezi ya Programu ya Pili ya Kukuza Ujuzi na Stadi za Kazi (ESPJ II)

Na.Mwandishi Wetu.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo, amesema Programu ya Pili ya Kukuza Ujuzi na Stadi za Kazi (ESPJ II) ni hatua ya kimkakati inayolenga kuongeza ajira zenye tija na kuimarisha ustawi wa jamii.

Akizungumza Julai 31, 2026 Jijini Dar es Salaam wakati akifungua Kikao cha Kamati Elekezi ya Programu hiyo, Prof. Nombo amesema kuwa programu hiyo inalenga kuzalisha rasilimali watu wenye umahiri wa kisasa kwa sekta za viwanda, teknolojia, ubunifu na sekta binafsi, ili kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.

Prof. Nombo amebainisha kuwa Programu imeandaliwa katika misingi ya Mkakati wa Pili wa Taifa wa Kuendeleza Ujuzi, Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014 Toleo la 2023, pamoja na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Katibu Mkuu huyo amesisitiza kuwa matokeo makuu yanayotarajiwa ni kuongeza fursa za mafunzo kwa vijana wasio na ajira na wanaotoka katika mazingira magumu, kuimarisha mfumo wa kusimamia Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (TVET), na kushirikisha sekta binafsi katika kuboresha ubora wa mafunzo.

Kwa upande wake, Mratibu wa Programu ya Pili ya Kukuza Ujuzi na Stadi za Kazi, Dkt. Erick Mgaya, amesema utekelezaji wa Programu hiyo ni wa miaka sita wenye thamani ya Shilingi bilioni 780 sawa na Dola za Kimarekani milioni 300 unatarajiwa kunufaisha zaidi ya Watanzania milioni moja.

Amefafanua kuwa programu hii inatekelezwa na Taasisi 19 pamoja na wizara mbalimbali ikiwemo Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wizara ya Afya, Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI, Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano, pamoja na taasisi za mafunzo zikishirikiana na Sekta binafsi.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiagana na viongozi mbalimbali kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam kabla ya kuondoka nchini, kuelekea Luanda, Angola ambapo anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika hafla ya Uzinduzi wa Hospitali iliyopewa jina la Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, tarehe 31 Julai,2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Mama Maria Nyerere muda mfupi kabla ya kuanza safari ya kuelekea Luanda, Angola ambapo anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika hafla ya Uzinduzi wa Hospitali iliyopewa jina la Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, tarehe 31 Julai, 2026.

Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Mfumo wa Stakabadhi za Ghala umeendelea kuonyesha mafanikio makubwa nchini baada ya kuwawezesha wakulima na wazalishaji kuingiza zaidi ya Shilingi trilioni 2.2 kupitia mauzo ya mazao katika mwaka wa fedha 2025/2026, huku kiasi cha mazao yaliyouzwa kupitia mfumo huo kikiongezeka kwa asilimia 43.6 ikilinganishwa na mwaka uliopita.

Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari leo jijini Dodoma kuhusu utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) kwa mwaka wa fedha 2025/2026 na mwelekeo wa mwaka wa fedha 2026/2027, Mkurugenzi Mtendaji wa WRRB,  Asangye Bangu, amesema mafanikio hayo yanaakisi kuongezeka kwa imani ya wakulima na wadau katika matumizi ya mfumo huo.

Amesema Mfumo wa Stakabadhi za Ghala ulianza kutekelezwa kwa zao la korosho pekee, lakini kwa sasa umejumuisha mazao na bidhaa 18, ikiwemo kahawa, kakao, ufuta, soya, mbaazi, dengu, choroko, mahindi, mpunga, mchele, chai, maharage, karanga, asali, mihogo na vitunguu swaumu. Aidha, mfumo huo sasa unatekelezwa katika mikoa 23 nchini, hatua inayoonesha kupanuka kwa wigo wa huduma na kuimarika kwa masoko ya mazao.

 Bangu amesema katika mwaka wa fedha 2025/2026 Serikali ilitoa Shilingi milioni 950 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya WRRB. Fedha hizo zilielekezwa katika utoaji wa elimu na uhamasishaji kwa wakulima na wadau, uboreshaji wa miundombinu ya TEHAMA na mifumo ya kidijitali, kuimarisha ukaguzi na usimamizi wa maghala pamoja na ununuzi wa vitendea kazi vilivyoongeza ufanisi wa taasisi hiyo.

Ameeleza kuwa uwekezaji huo umeimarisha uwezo wa WRRB kusimamia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala kwa ufanisi zaidi na kuongeza upatikanaji wa huduma bora kwa wananchi.

Akifafanua mafanikio ya mfumo huo, amesema jumla ya kilo 1,122,246,475 za mazao tisa ambayo ni korosho, ufuta, kahawa, kakao, mbaazi, dengu, choroko, soya na chai ziliuzwa kupitia minada ya kidijitali inayosimamiwa na Soko la Bidhaa Tanzania (TMX), ikilinganishwa na kilo 781,659,285 zilizouzwa mwaka uliotangulia.

"Ongezeko hili la zaidi ya kilo milioni 340 ndani ya mwaka mmoja linaonesha kuwa wakulima wengi zaidi wanaendelea kuuamini Mfumo wa Stakabadhi za Ghala kutokana na uwazi, ushindani wa bei na uhakika wa soko unaopatikana kupitia mfumo huu," amesema.

Kutokana na mauzo hayo, wakulima na wauzaji walilipwa jumla ya Shilingi trilioni 2.298, huku Serikali za Mitaa zikikusanya Shilingi bilioni 61.05 kupitia ushuru wa mazao (CESS). Aidha, thamani ya biashara yote iliyofanyika kupitia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala ilifikia Shilingi trilioni 2.679.

 Bangu amesema fedha zilizowafikia wakulima zimechangia kuinua uchumi wa kaya kwa kuwawezesha kumudu gharama za elimu, afya, makazi na kuongeza uwekezaji katika shughuli za uzalishaji.

Aidha, amesema mapato yaliyopatikana kupitia ushuru wa mazao yameziwezesha Halmashauri kuimarisha utoaji wa huduma za jamii kwa kuwekeza katika ujenzi na ukarabati wa barabara, shule, vituo vya afya, masoko na miundombinu mingine muhimu inayowanufaisha wananchi.





NA DENIS MLOWE, IRINGA


WAKALA Mkuu wa mbegu za Taasisi ya ASA mkoani Iringa, Kampuni ya Mgongolwa Agrovet & Seeds Company Limited, imewahimiza wakulima kutumia mbegu bora zinazozalishwa na Taasisi ya ASA ili kuongeza uzalishaji wa mazao na kuondokana na changamoto ya kutumia mbegu zisizo na ubora.

Akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi za Iringa Press Club, Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Joseph Saidi Mgongolwa, alisema wamepewa dhamana na Taasisi ya ASA iliyo chini ya Wizara ya Kilimo kuhakikisha mbegu bora zinawafikia wakulima wa vijijini na mijini kwa wakati kabla ya kuanza kwa msimu wa kilimo.

Alisema hatua hiyo ni sehemu ya maandalizi kuelekea maadhimisho ya Siku ya Wakulima (Nanenane), huku lengo likiwa kuwafikishia wakulima mbegu zenye ubora wa hali ya juu kwa bei nafuu ili kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao.

Mgongolwa alisema Taasisi ya ASA imeamua kusogeza huduma karibu na wakulima kupitia mawakala wake ili kuhakikisha kila mkulima, mdogo na mkubwa, anapata mbegu bora zinazokidhi mahitaji ya maeneo mbalimbali ya kilimo nchini.
Alieleza kuwa kampuni hiyo itasambaza mbegu za mahindi zinazofaa kwa maeneo yenye mvua chache na maeneo yenye mvua nyingi, pamoja na mbegu za mpunga, alizeti na maharage ya njano na mekundu.

"Tunawaomba wakulima wa mkoa wa Iringa na Watanzania kwa ujumla kuamini mbegu za ASA ambazo zinazalishwa chini ya Wizara ya Kilimo. Mbegu hizi zimeonyesha uwezo mkubwa wa kuongeza mavuno na zinapatikana kwa bei nafuu ili kumwezesha mkulima kupata tija zaidi," alisema.

Aidha alisema kampuni hiyo imejipanga kufungua vituo vya usambazaji katika maeneo mbalimbali ya vijijini ili kurahisisha upatikanaji wa mbegu hizo, huku duka kuu likiwa katika eneo la CCM Mkoa wa Iringa.

Mgongolwa alisema moja ya changamoto kubwa iliyokuwa ikiwakabili wakulima ni uwepo wa mbegu feki, hali iliyosababisha wengi kupata hasara kutokana na mavuno hafifu.

Alisema kampuni yake itahakikisha mbegu zote zinazosambazwa ni halisi kutoka Taasisi ya ASA na zitakuwa na alama maalumu za utambuzi ikiwemo nembo ya Taifa ili kuondoa uwezekano wa wakulima kununua mbegu bandia.

"Nami ni mkulima na nimewahi kutumia mbegu mbalimbali baada ya kutumia mbegu za ASA nilishuhudia ongezeko kubwa la mavuno, ndiyo maana ninawahamasisha wakulima wenzangu kuzitumia kwa maendeleo ya kilimo chetu," alisema.

Kwa upande wa sifa za baadhi ya mbegu, alisema mbegu ya mahindi aina ya T105 hustawi katika maeneo yenye urefu wa mita 800 hadi 1,500 kutoka usawa wa bahari, hukomaa ndani ya siku 105 hadi 115 na inaweza kutoa magunia 18 hadi 22 kwa ekari endapo mkulima atazingatia kanuni bora za kilimo.

Aliongeza kuwa mbegu ya mpunga aina ya TXD 306 (Saro 5) imekusudiwa kwa maeneo ya mabondeni na skimu za umwagiliaji, hukomaa ndani ya siku 110 hadi 120, huku ikiwa na sifa ya kutoa mchele usiovunjika kirahisi wakati wa kukobolewa na wenye harufu nzuri.

Kwa mbegu ya alizeti aina ya Record, alisema hustawi katika maeneo yenye urefu wa mita 0 hadi 2,400 kutoka usawa wa bahari, hukomaa ndani ya siku 110 hadi 120 na inaweza kutoa mavuno ya kilo 600 hadi 800 kwa ekari, ikiwa na kiwango cha mafuta kati ya asilimia 32 na 48.

Mgongolwa alitoa wito kwa wakulima kutumia mbegu bora zilizoidhinishwa na serikali ili kuongeza uzalishaji wa mazao, kuimarisha usalama wa chakula na kuongeza kipato cha kaya kupitia kilimo chenye tija.



▪️Atoa siku 14 Kituo cha Kitaifa cha Oparesheni kianze kufanya kazi

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba ametoa siku 14 kwa wizara na taasisi zinazohusika na Kituo cha Kitaifa cha pamoja cha Oparesheni zipeleke wawakilishi ili kianze kufanya kazi mara moja.

"Wizara na taasisi zote zinazohusika na utekelezaji wa majukumu katika Kituo cha Kitaifa cha pamoja cha Oparesheni zipeleke wawakilishi wote wanaohitajika ndani ya siku 14 kuanzia leo. Kituo hiki kianze kazi mara moja ili kuleta tija inayokusudiwa," amesema Waziri Mkuu.

Dkt. Mwigulu ametoa wito huo leo (Ijumaa, Julai 31, 2026) wakati akizungumza na washiriki wa hafla ya makabidhiano na uzinduzi wa boti mbili za doria aina ya PB Sailfish 02 na PB Sailfish 03 iliyofanyika bandarini, jijini Dar es Salaam. Boti hizo zimenunuliwa kwa thamani ya dola za Marekani milioni 1.6.

Amezitaka Wizara za Muungano zinazohusika na suala hilo zishirikiane ili kuziba chochoro zote ambazo zingetumiwa na wahalifu katika eneo hili tunalolilenga na hasa katika mipaka ya mwambao wa bahari.

Ili kuhakikisha boti hizo zinafanya kazi kama inavyotarajiwa, Waziri Mkuu ameziagiza wizara na taasisi zote za umma zinazohusika katika matumizi ya boti hizi za doria zitenge fedha kwa ajili ya kazi za boti hizi.

"Ninasisitiza suala la kutenga bajeti ili kazi za doria zisikwamishwe na ukosefu wa bajeti. Nimekuwa nikikutana na kesi kama hizo mikoani ambapo Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan alinunua ambulance za kisasa na nyingine zina ICU lakini zinashindwa kuhudumia wagonjwa kwa wakati kwa kukosa mafuta. Hili linakinzana na dhamira njema ya Mheshimiwa Rais ya kutaka kuokoa maisha ya Watanzania pindi wanahitaji huduma hizo," amefafanua.

Akielezea umuhimu wa boti hizo za doria, Waziri Mkuu amesema makabidhiano ya boti hizo ni tukio muhimu kiuchumi kwa sababu zinaenda kulinda mazao yatokanayo na uchumi wa bluu. Amesema uhitaji wa boti hizo umekuwa ni kilio cha muda mrefu tangu yeye akiwa Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi.

Amesema upatikanaji wa boti hizo mbili, utaimarisha ulinzi hasa ikizingatiwa kwamba Tanzania ni lango la nchi nyingi zikiwemo za Afrika Mashariki na za SADC lakini usalama utakaokuwepo unahusu Tanzania na wananchi wa hizo nchi jirani. "Wananchi kutoka nchi hizo watakuwa na uhakika wa usalama watakapotumia lango la bandari ya Dar es Salaam," amesisitiza.

Mapema, akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na washiriki wa hafla hiyo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Prof. Palamagamba Kabudi alisema ununuzi wa boti mbili za doria aina ya PB Sailfish 02 na PB Sailfish 03 ulifanyika baada ya kukamilika kwa taratibu zote za manunuzi ambapo mkataba wa ununuzi ulisainiwa Julai 29, 2025 kati ya Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini na Kampuni ya Yamaha Motors Co. Ltd.

“Ujenzi wa boti hizo ulifanyika nchini Japan kwa kuzingatia vipimo na viwango vya kimataifa vilivyokubaliwa na wataalamu wa Serikali. Hadi kukamilika kwake, ujumbe wa wataalamu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, TASAC, UNDP na Chuo cha Mipango ulifanya ziara za ukaguzi ili kujiridhisha na ubora wa kazi iliyotekelezwa,” alisema.

Naye, Balozi wa Japan nchini Tanzania, Mikami Yoichi alisema kijiografia Tanzania na Japan ziko mbali lakini zinaunganishwa na bahari za Hindi na Pasifiki na kwamba uwepo wa usalama kwenye mipaka ya baharini, kuwahakikishia wananchi wake usalama wa maisha yao.

Alisema ana imani kwamba Serikali ya Tanzania itahakikisha boti hizo zinatumika kwa miaka mingi kwa faida ya vizazi vijavyo.












 WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,  Dkt. Mwigulu  Nchemba, amesema Serikali chini ya uongozi wa Rais. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuweka mazingira wezeshi ya kukuza vipaji vya vijana kupitia uwekezaji katika sekta ya michezo na ujenzi wa miundombinu ya kisasa.

Akizungumza usiku wa kuamkia  leo,  Julai 31 2026 wakati  tamasha la mchezo wa Masumbwi “Knockout ya Mama Season 9” liliofanyika katika ukumbi wa The super Dome  Masaki jijini Dar es Salaam, Waziri Mkuu amesisitiza mpango wa  Serikali kujenga arena kubwa ya kisasa itakayokuwa kitovu cha matukio mbalimbali ya michezo na burudani nchini.

Amesema Rais  Samia Suluhu Hassan anaendelea kuunga mkono juhudi za vijana na wadau wa michezo nchini, huku Serikali ikiendelea kushirikiana kwa karibu na sekta binafsi katika kuimarisha maendeleo ya michezo na kuibua vipaji.




 KUNA wakati kama binafamu wenye akili timamu lazima tutafakari mambo yanayoendelea nchini na kwa siku ya leo tujadili kidogo kuhusu michango ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA).


Ndio lazima tujadili maana imekuwa gumzo kila kila kona, sio kwasababu michango inadaiwa kutafunwa na baadhi ya viongozi wa Chama hicho, hapana.Nazungumzia kuhusu kusuasusa kwa michango yenyewe.

Ni kama wachangiaji wameshutuka kwamba fedha wanazotoa zinaliwa na wajanja wachache lakini kubwa zaidi waliokuwa wanakichangia kwa muda mrefu wakiwemo wafanyabishara wameona chama hicho kimepoteza muelekeo,hakina mvuto.

Ile Kampeni ya Tonetone ya kuchangia CHADEMA imedoda kabisa .Na hivi karibuni tumesikia tuhuma za michango kutafunwa na wachache.

Hata hivyo katika hili la michango ya CHADEMA kuonekana inasuasua ni vema kwanza tukarudi mwanzo kule wakati Chama hicho kimeanza mwaka 1992 baada ya kuanza kwa Mfumo wa Vyama vingi nchini Tanzania.

Wakati chama hicho kinaanza waanzilishi wake walikuwa mchanganyiko wa wanasiasa, wanaharakati, watu maarufu na wa sekta binafsi waliotaka mfumo wa kisiasa unaoweka msisitizo katika uwajibikaji na uhuru wa kiuchumi.

Miongoni mwa watu wa mwanzo kabisa wakatiCHADEMA inaanza walikuwepo akina Edwin Mtei(sasa marehemu)Mwanasheria mashuhuri Bob Makani na wengine wengi.Hata Ndesamburo naye ni miongoni mwao.

Ukweli watu hao wa mwanzo kabisa hawakuwa wanamapinduzi, bali walikuwa wanakapitalisti waliochoshwa na uendeshaji wa Serikali ya wakati huo.

Kutokana na mipango na mikakati ya CHADEMA kwa wakati ule ilishuhudiwa wafadhili wa awali wengi wao wakiwa ni wafanyabiashara na sekta binafsi.

Katika miaka ya mwanzo, CHADEMA ilivutia msaada wa watu wenye uwezo na wafanyabiashara waliotaka sera zinazorahisisha biashara na uwekezaji.

Michango hiyo mara nyingi haikuonekana hadharani; ilitolewa kwa njia za ndani au kwa msaada wa kimkakati ili kuimarisha miundombinu ya chama na kampeni za kukujenga chama mikoani. Kujiunga kwa viongozi wenye umaarufu kuliongeza mvuto wa chama kwa wafadhili na wafuasi.

Pia ilikuwa ni jambo la kawaida kusikia Mfanyabiashara maarufu Mustafa Jafari Sabodo (sasa marehemu) akitoa mamilioni ya fedha kwa Chama hicho na ndoto yake ilikuwa ni kuona Chama hicho kinakuwa na Ofisi yake.

Ndoto ya Sabodo haikutimia maana licha ya kutoa zaidi ya milioni 100 hazikutumika kujenga ofisi.Sijui zilitumika wapi? Zile fedha hazikujulikana zilikwenda wapi.CHADEMA bwana wajanja wajanja sana.

Ukweli katika miaka 1995 mpaka miaka ya 2010 CHADEMA ilikua kwa kasi kubwa na mwaka 2014 baada ya Edward Lowassa alipotangaza kujiunga na Chama hicho kikakua zaidi.Tukashuhudia gumzo kubwa kwa chama hicho na umaarufu mkubwa katika historia ya siasa za vyama vingi nchini Tanzania.

Kujiunga kwake Lowasa kulionyesha uwezo wa CHADEMA kuvutia viongozi wa ngazi ya juu kutoka upande wa pili wa kisiasa. Mabepari walifungua mikoba yao, wakimimina fedha nyingi kuunga mkono chama.

Hata hivyo, kila kitu kilibadilika baada ya kuingia kwa uongozi mpya wa Tundu Lissu. Uongozi wake na wa viongozi wenzake wa kisiasa uliashiria mabadiliko ya mkazo wa chama kuelekea masuala ya haki za kiraia, uwazi, na masuala ya kijamii.

Hiyo ilileta mabadiliko ya mtazamo wa chama ambayo baadhi ya wafadhili waliona hayakuwa ya kuendeleza maslahi ya kiuchumi.

Pamoja nayo hayo tangu CHADEMA ilipofanya mabadiliko ya uongozi wake wa ngazi za kuu tunashuhudia athari na changamoto za mabadiliko hayo.

Mabadiliko hayo ya mwelekeo wa chama yameathiri pia chanzo cha ufadhili kwa operesheni za CHADEMA kwenye nyanja kadhaa. Ni wazi CHADEMA imepoteza uaminifu wa wafadhili wa sekta binafsi.

Haswa kundi la wafanyabiashara wanaotaka sera za soko huria wamesita kuendelea kutoa michango baada ya chama kuoonyesha msimamo wakisoshalisti au kinachokosoa tu sekta binafsi bila kujaribukuelewa changamoto zao.

Upungufu wa rasilimali za kampeni umeonekana wazi, bila michango kubwa, chama kinakosa uwezo wa kuendesha kampeni za kitaifa, kulipa miundombinu ya chama, na kumudu gharama za kisheria na mahitaji ya wanachama.

Hizo ni baadhi ya atahari za madiliko yaliyotokana na chama kilijikita na wanaharakati ambao wanaamini"wafanyabiashara hawana shida." Mabadiliko ya mwelekeo bila mkakati wa kuunganisha tabaka tofauti za wafuasi(wafanyabiashara, wanaharakati, wanasiasa wa jadi) umeacaha pengo la utekelezaji.

CHADEMA sasa inahitaji sera zinazoonyesha jinsi masuala ya kijamii (kama kupunguza umaskini) yanavyoweza kuendana na sera za kukuza biashara ili kuwashirikishawafadhili na wafuasi kwa pamoja.

Wafanyabiashara na wawekezaji wanaotazama uongozi huo wanaona chama kinachobeza matatizo yao na kuwafanya kuwa maadui. Kwa nini mfanyabiashara awekeze kwenye chama kinachomtukana?

Kwanini awekeze kwenye Chama ambacho kinahubiri shari badala ya heri.Kwanini Mfanyabiashara awekeze katika chama ambacho kutwa kuchwa kiko barabarani kina uhubiri chuki na mipasuko katika jamii?


Na Mwandishi Wetu
MKURUGENZI Mtendaji wa Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP-CENTRE), David Kafulila, amesema kuwa mfumo wa ubia kati ya Serikali na Sekta Binafsi (PPP) si jambo la hiari au la kufikirika tu, bali ni mkakati madhubuti wa kimfumo unaolenga kuikomboa nchi kiuchumi na kuongeza ufanisi wa utendaji katika sekta mbalimbali.

Kafulila alibainisha hayo Alhamisi, Julai 30, 2026, wakati akihutubia wataalamu, wasomi, na wadau wa usafirishaji katika Kongamano la Mwaka la Chama cha Wataalamu wa Lojistiki na Usafirishaji Tanzania (CILT), lililofanyika katika Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), Mabibo jijini Dar es Salaam.

Akichambua umuhimu wa mfumo huo, Kafulila alieleza kuwa mataifa mengi duniani yanageukia mifumo ya ubia kwa sababu kuu tatu ambazo ni kuvuta mitaji kutoka sekta binafsi, kuingiza teknolojia ya kisasa, na kuimarisha ufanisi wa usimamizi (management efficiency).

Alisisitiza kuwa uchumi wa sasa unategemea zaidi maarifa na ujuzi kuliko rasilimali za asili pekee.

"Ushirikiano wa kiuchumi kati ya Serikali na Sekta Binafsi (PPP) si jambo la hiari au la kuota, bali ni mkakati wa makusudi na wa kimfumo wa kuikomboa nchi kiuchumi na kuongeza ufanisi wa utendaji,” alisema.

“Serikali haiwezi kujenga kila kitu kuanzia bandari, reli, barabara, masoko na stendi, na wakati huo huo ikawa na fedha za kujenga watu wenye ubora wa kushindana duniani," aliongea.

Alibainisha kuwa kupitia PPP, serikali inajipa nafasi ya kuachia sekta binafsi maeneo ya kibiashara ili kuokoa fedha ambazo zinatumika kwenye uwekezaji mkubwa wa rasilimali watu kupitia elimu bora.

Katika kongamano hilo, Waziri Mkuu, Dk Mwigulu Nchemba, alijibu ombi la Mkuu wa Chuo cha NIT, Dk Prosper Mgaya, kuhusu changamoto ya ukosefu wa mikopo kwa wanafunzi wanaochukua kozi za muda mfupi za kiufundi.

Dk Nchemba aliwahakikishia washiriki kuwa serikali imepokea ombi hilo kwa uzito mkubwa, akisema kuwa utaalamu katika fani za lojistiki na ufundi ni nguzo muhimu kwa maendeleo ya taifa.

"Serikali imepokea kwa uzito changamoto hiyo. Kozi za ufundi na lojistiki zinahitaji utimamu wa akili na uwezo wa mwanafunzi bila kujali hali ya kiuchumi ya familia anayotoka,” alisema Dk Nchemba.

“Serikali itaangalia mbinu mbadala ya kuwatengenezea mfumo rafiki wanafunzi wa kozi hizo za ufundi ili kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo," alisisitia.
Dkt. Nchemba alitolea mfano wa mfumo wa Samia Scholarship ambao umekuwa ukizingatia ufaulu na uwezo wa kitaaluma badala ya kigezo cha umaskini pekee, akiahidi kuwa serikali itaendelea kuboresha mazingira ya upatikanaji wa elimu ya ufundi nchini.

Kongamano hilo limeonekana kuwa jukwaa muhimu la kuunganisha sekta ya usafirishaji na mikakati mipana ya kiuchumi ya nchi kwa miaka 25 ijayo.


Na Mwandishi Wetu
SERIKALI imeiagiza Wizara ya Uchukuzi kuharakisha taratibu za kuwasilisha Waraka wa Baraza la Mawaziri ili kuwezesha kuanzishwa kwa Bodi ya Usajili wa Wataalamu wa Lojistiki na Usafirishaji, hatua inayolenga kuimarisha ubora, weledi na uwajibikaji wa wataalamu wa sekta hiyo nchini.

Akifungua Kongamano la Wataalamu wa Lojistiki na Usafirishaji katika Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) jijini Dar es Salaam leo, Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali imepokea mapendekezo ya wadau wa sekta hiyo na itaendelea kuyafanyia kazi, ikiwemo kushirikiana na Ofisi ya Rais–Utumishi na TAMISEMI kutathmini uanzishwaji wa vitengo maalumu vya maafisa wa lojistiki na usafirishaji katika taasisi za umma.

Dkt. Nchemba amesema Serikali itaendelea kuwekeza katika miundombinu ya uchukuzi na kuimarisha Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) kwa kuongeza bajeti na kuhakikisha fedha zilizoidhinishwa zinatolewa kwa wakati. Pia amesema itaendelea kutathmini uwezekano wa kuwajumuisha wanafunzi wa programu maalumu za chuo hicho katika mfumo wa mikopo ya elimu ya juu kadri hali ya kifedha itakavyoruhusu.

Naibu Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile, amesema mafanikio ya sekta ya uchukuzi yametokana na uwekezaji wa Serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika reli ya kisasa (SGR), bandari, viwanja vya ndege na vyuo vya mafunzo, hatua zilizoongeza mchango wa sekta hiyo katika uchumi wa taifa na kuongeza uwezo wa bandari za Dar es Salaam, Tanga na Mtwara kuhudumia mizigo.

Kihenzile amesema mapato yatokanayo na maboresho hayo yamewezesha Serikali kuendelea kuimarisha NIT kwa kujenga mabweni, kununua vifaa vya kisasa vya kufundishia na kuboresha miundombinu ya mafunzo ya marubani, wahandisi wa ndege na wataalamu wengine wa lojistiki na usafirishaji.

Kwa upande wake, Rais wa Chama cha Wataalamu wa Lojistiki na Usafirishaji Tanzania (TALTA), Alphonce Mwingila, ameiomba Serikali kuweka mkakati madhubuti wa kuboresha mfumo wa ukaguzi na matengenezo ya magari ya mafunzo ya udereva ili kupunguza gharama zinazowakabili wamiliki wa shule za udereva.

«"Kuna msemo wa Kiingereza unasema, If you fail to plan, you are planning to fail. Tunahitaji mipango mizuri katika eneo hili. Baadhi ya magari yanapotoka TEMESA baada ya kufanyiwa ukaguzi yanakuwa na matatizo mapya kabisa, hivyo mmiliki analazimika kurudi tena kuyafanyia matengenezo na gharama zinakuwa kubwa kuliko uhalisia," amesema Mwingila.»

Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), Dkt. Prosper Mgaya, amesema ziara ya Waziri Mkuu chuoni hapo imeandika historia kwa kuwa ni mara ya kwanza kwa Waziri Mkuu kutembelea taasisi hiyo tangu ilipoanzishwa. Amesema mafanikio hayo yametokana na uwekezaji wa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ikiwemo kutenga takribani Sh bilioni 70 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Umahiri cha Mafunzo ya Usafiri wa Anga.

Dkt. Mgaya amesema NIT imeendelea kujiimarisha kwa kutoa mafunzo katika modi zote tano za usafiri na kuboresha mitaala yake ili kuzalisha wataalamu wenye ushindani ndani na nje ya nchi, huku baadhi ya wahitimu wake wakiajiriwa na Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) na Air Dubai.

Aidha, amesema mafunzo ya urubani yameimarika baada ya Serikali kununua ndege za mafunzo, ambapo hadi sasa wanafunzi wanne wamehitimu urubani na wanane wako katika hatua ya kuruka peke yao (solo). Ameongeza kuwa NIT itaendelea kushirikiana na TALTA kuboresha mitaala ili iendane na mahitaji ya soko la ajira.Nikiihariri zaidi, inaweza kufupishwa hadi mtindo wa habari ya gazeti wenye paragrafu 8 bila kupoteza hoja kuu.













 


Top News