*Kambi maalum inaanza Jumatatu hadi Septemba 11

Na Mwandishi Wetu
HOSPITALI ya Shifaa Pan African ya Kinondoni jijini Dar es Salaam imeandaa kambi maalum kufanya upasuaji wa kupunguza uzito kwa kutumia matundu madogo kuanzia Agosti 31 mpaka Septemba 11.

 Daktari bingwa wa upasuaji wa hospitali hiyo, Kassim Bahsan alisema jana kuwa kambi hiyo itafanyika katika hospitali hiyo kuanzia Agosti 31 mwezi huu hadi Septemba 11.

Alisema katika kambi hiyo wananchi watapata fursa ya kufanyiwa tathmini ya mwili na kupata ushauri wa kitaalamu wa upasuaji wa kupunguza uzito kwa kutumia teknolojia ya kisasa ya matundu madogo.

“Kama umekuwa ukipambana na unene kupita kiasi na unatafuta njia salama na yenye ufanisi ya kuboresha afya yako hii ni fursa muhimu ya kuchukua hatua kuelekea maisha yenye afya bora,” alisema Dk Bahsan

Alisema tarehe 4 mwezi Septemba hospitali ya Shifaa itaendesha mdahalo wa elimu kwa umma ambapo wananchi wote wanalikwa kushiriki kupata uelewa wa upasuaji wa kupunguza uzito.


“Ni semina ya elimu ya kupunguza uzito, watafahamu ni kwanini na nani ni mnufaika wa upasuaji huu watu watajifunza na watasikia ushuhuda kwa watu waliofanyiwa upasuaji na kupungua uzito, wengine wameacha dozi za kisukari, maumivu ya nyonga yameisha,” alisema

Naye Mkuu wa Idara ya Upasuaji hospitalini hapo, Dk Murad Tarmohamed alisema hiyo ni fursa kwa watu wenye matatizo ya uzito uliopitiliza kwani wanaweza kurejea kwenye maisha yao ya kawaida baada ya upasuaji.

“Wananchi waitumie hii fursa kukutana na madaktari bingwa wabobezi kwenye upasuaji ambao watawashauri hatua za kuchukua kabla ya upasuaji ili wafanyiwe matibabu yatakayowarejesha kwenye maisha ya kawaida,” alisema

“Uzuri ni kwamba upasuaji huu unafanywa kwa njia ya matundu madogo ambao unamwezesha mtu aliyefanyiwa matibabu kupona haraka na kuendelea na shughuli zake za kila siku,” alisema

Aidha, alisema kuna ushuhuda wa baadhi ya watu waliofanyiwa upasuaji kwenye hospitali hiyo wakiwa na uzito wa hadi kilo 148 na kufanikiwa kurudi kwenye kilo 98 ambao kwa sasa wanaishi maisha bora wakiwa wameondokana na uzito uliopitiliza.

Hospitali hiyo imeshawafanyia upasuaji wa kupunguza uzito ambao umekuwa wa wenye mafanikio kwa kutumia tundu dogo watu 20 waliokuwa na uzito mkubwa.

Daktari bingwa wa upasuaji wa hospitali hiyo, Murad Tarmohamed, alisema hospitali hiyo imeweka wataalamu bobezi kwa ajili ya taaluma hiyo.

“Watu wengi wanadhani kuwa upasuaji huu ni kwaajili ya urembo hapana, unafaida nyingi sana kama kuepuka magonjwa ya sukari na wakishafanyiwa wakapona kabisa, kuna watu wanakosa pumzi sababu ya uzito mkubwa wakifanyiwa wanapona,” alisema

Alisema kuna watu ambao wanapata shida ya magoti na nyonga sababu ya maumivu wanayopata wanapotembea lakini wakifanyiwa upasuaji wanapona.

Alisema magonjwa kama ya moyo yanayotokana na uzito kuwa mkubwa yamekuwa yakiondoka kwa watu wanaofanyiwa huduma hiyo.

“Mtu anapofanyiwa upasuaji huu anakuwa na nguvu zaidi anarudi kwenye maisha ya kawaida, anaacha kuchoka mara kwa mara anakuwa anafanya shughuli zake kama zamani, tunasisitiza ni muhimu sana si kwa muonekano bali kwa ajili ya afya ya mhusika,” alisema

“Umuhimu wa upasuaji kama huu ni shida ambazo unaondokana nazo baaada ya upasuaji kama moyo, sukari, presha sukari, maumivu ya nyonga, magoti  na kukosa pumzi ukiwa umelala,” alisema hiyo ni kambi ya tatu kufanya hospitali ya Shifaa

“Faida ya upasuaji huu ni kwamba mgonjwa hakai sana hospitalini, akifanyiwa leo kesho anatoka anakwenda nyumbani kuendelea na maisha yake kama kawaida,” alisema

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026, Ndugu Wazo Michael Mwang’onda, leo tarehe 28 Agosti 2026 ametembelea na kuzungumza na wafanyabiashara katika Hoteli ya KER iliyopo Mtaa wa Butambala, Kata ya Igulwa Wilaya ya Bukombe.

Ziara hiyo ni sehemu ya Programu ya Nishati Safi na Salama ya Kupikia inayotekelezwa na Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan. Lengo ni kuhamasisha matumizi ya nishati safi katika hoteli na migahawa.

Akizungumza na wamiliki na wafanyakazi wa Hoteli ya KER, Mwang’onda amesema Serikali ina dhamira ya kuwawezesha wafanyabiashara wa vyakula kutumia nishati safi ili kupunguza gharama za uendeshaji na kuboresha mazingira ya kazi.

Amesema matumizi ya nishati safi kama gesi ni ya ufanisi zaidi, yanaokoa muda na yana afya kuliko kutumia kuni na mkaa. Hii inawasaidia mama lishe na baba lishe kuongeza kipato chao kwa sababu gharama zinapungua na huduma inakuwa ya haraka.

Mwang’onda pia amesisitiza umuhimu wa kulinda mazingira. Amesema kupunguza matumizi ya kuni na mkaa kutaokoa misitu na kusaidia kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi.

Ameipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Bukombe kwa kuwekeza katika kuhamasisha wananchi kuhamia nishati safi kupitia mapato yake ya ndani. Amesema hatua hiyo inaonyesha nia ya dhati ya Serikali ya Mitaa kuleta maendeleo.

Wafanyabiashara wa Hoteli ya KER wamemshukuru Kiongozi wa Mwenge kwa ziara hiyo na wameahidi kuzingatia matumizi ya nishati safi katika shughuli zao za kila siku. Wamesema wamepata elimu ya namna ya kupika kwa usalama na kwa haraka.

Mwishoni Mwang’onda amewataka wafanyabiashara wengine wilayani Bukombe kuiga mfano wa Hoteli ya KER na kuanza kutumia nishati safi. Amesema kwa kufanya hivyo Tanzania itakuwa imepiga hatua kubwa katika kuhifadhi mazingira na kuboresha afya ya wananchi.








 WANANCHI waliotembelea banda la Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA) katika Maonesho ya Utamaduni, wameeleza kufurahishwa na elimu wanayoipata kuhusu majukumu ya Wakala katika kuratibu uagizaji wa mafuta kwa pamoja na kuhakikisha upatikanaji wa mafuta nchini.

Wananchi hao wamesema maonesho hayo yamekuwa fursa muhimu kwao kupata uelewa kuhusu Mfumo wa Uagizaji wa Mafuta kwa Pamoja (Bulk Procurement System – BPS), namna mafuta yanavyoagizwa nchini na nafasi ya PBPA katika kuratibu mchakato huo.

Bi. Maria Ngilisho, mmoja wa waliotembelea banda hilo, alisema elimu hiyo imemsaidia kuelewa mchakato wa upatikanaji wa mafuta nchini, ambao awali hakuwa na ufahamu wa kutosha kuuhusu.

“Nimefurahi kupata elimu hii kwa sababu tumekuwa tukitumia mafuta kila siku, lakini hatukuwa tunafahamu mchakato unaofanyika hadi mafuta yanapofika nchini. Sasa nimeelewa kuwa kuna taasisi kama PBPA inayoratibu uagizaji wa mafuta kwa pamoja,” alisema Ngilisho.

Naye, Bw. Michael Maganga, alisema mawasiliano ya ana kwa ana na watumishi wa PBPA yamewapa wananchi nafasi ya kuuliza maswali na kupata ufafanuzi wa moja kwa moja kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu mafuta.

“Elimu tunayopata hapa ni muhimu sana kwa sababu tunapata nafasi ya kuuliza maswali yanayotuhusu kama watumiaji wa mafuta na tunapata majibu kutoka kwa wataalamu. Ni vizuri PBPA kuendelea kutumia maonesho haya kuwafikia wananchi,” alisema Maganga.

Kwa mujibu wa PBPA, miongoni mwa majukumu ya Wakala ni kukusanya mahitaji ya mafuta kutoka kwa kampuni za uuzaji wa mafuta, kuendesha zabuni za kimataifa za ununuzi wa mafuta kwa wingi, pamoja na kuratibu upokeaji na uwasilishaji wa bidhaa hizo nchini. Ushiriki wa PBPA katika maonesho mbalimbali ni sehemu ya juhudi za Wakala za kuwaelimisha

Ushiriki wa PBPA katika maonesho mbalimbali ni sehemu ya juhudi za Wakala za kuwaelimisha wananchi kuhusu majukumu yake na nafasi yake katika sekta ya mafuta, huku ukitoa fursa kwa wananchi kupata ufafanuzi kuhusu mchakato wa uagizaji wa mafuta na hatua zinazochukuliwa kuhakikisha upatikanaji wa bidhaa hizo unaendelea kuwa wa uhakika nchini.
Naibu Spika wa Bunge, Daniel Baran Sillo, amesema Bunge lipo tayari kushirikiana na Serikali katika maandalizi ya AFCON PAMOJA 2027. Alitoa kauli hiyo wakati wa Bonanza la Bunge na NMB jijini Dodoma, lililoandaliwa na NMB Bank kwa kushirikiana na Bunge.

Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB, Filbert Mponzi, alisema benki hiyo imeandaa bonanza hilo kwa sababu michezo ina mchango katika afya na tija ya viongozi na watumishi. “Tunataka michezo iwe sehemu ya utamaduni wa kazi na huduma kwa wananchi,” alisema.

Mwenyekiti wa Bonanza la Bunge na Mbunge wa Makete, Festo Sanga, alisema tukio hilo limewakutanisha wabunge, wizara na taasisi mbalimbali, huku likitumika kuhamasisha mazoezi na mapambano dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza.

Mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki, Machano Ali Machano, alisema mashindano ya Mabunge ya Jumuiya ya Afrika Mashariki yatakayofanyika Arusha Desemba 2026 yatakuwa hatua nyingine ya kuimarisha michezo na ushirikiano wa kikanda.




















NA DENIS MLOWE IRINGA

WANAFUNZI wa zamani (Alumni) wa Shule ya Sekondari Tosa Maganga wameungana kuchangisha Shilingi milioni 250 kwa ajili ya ununuzi wa basi la shule hiyo, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya maadhimisho ya miaka 100 tangu kuanzishwa kwa shule hiyo.

Akizungumza kuhusu mpango huo, Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Grayson Nyamoga, ambaye ni mmoja wa wanafunzi waliowahi kusoma katika Shule ya Sekondari Tosamaganga amesema Alumni wamekubaliana kushirikiana kuhakikisha shule hiyo inapata basi litakalosaidia kuboresha mazingira ya kujifunzia na shughuli mbalimbali za shule.

Nyamoga amesema mahitaji yaliyobainishwa na shule ni pamoja na ukarabati wa Bweni la Mandela, ukarabati wa Bweni la Mapinduzi, ununuzi wa samani kwa ajili ya ukumbi wa chakula (dining hall), pamoja na ununuzi wa basi ambalo linakadiriwa kugharimu Shilingi milioni 250.

Amesema Alumni wameamua kuanza na jukumu la kuchangia fedha za ununuzi wa basi hilo, wakiamini kuwa ni sehemu ya kurejesha kwa jamii na shule iliyowapa msingi wa elimu wanafunzi hao ambao sasa wako katika kada mbalimbali ndani na nje ya Tanzania.

“Tunawahamasisha wana Tosa na Alumni wote tushirikiane kuchangia fedha hizi, Shilingi milioni 250, ili tuweze kununua basi hilo na kuwakabidhi vijana wetu na wadogo zetu waliopo pale Shule ya Sekondari Tosa Maganga,” amesema Nyamoga.

Amesema basi hilo linatarajiwa kuwa msaada mkubwa kwa wanafunzi na shule kwa ujumla, hasa katika kurahisisha usafiri wa wanafunzi wakati wa shughuli za kielimu, michezo, ziara za kitaaluma na shughuli nyingine zinazohitaji usafiri.

Nyamoga amesema hatua hiyo ni sehemu ya juhudi za Alumni kuhakikisha maadhimisho ya miaka 100 ya Shule ya Sekondari Tosa Maganga yanaacha alama ya kudumu kwa kizazi cha sasa na kijacho, badala ya kuwa sherehe pekee.

Maadhimisho ya miaka 100 ya Shule ya Sekondari Tosamaganga yanatarajiwa kufanyika kuanzia Oktoba 8 hadi 10, 2026, ambapo Alumni wanatarajiwa kushiriki katika shughuli mbalimbali zitakazolenga kuimarisha uhusiano kati ya shule na wanafunzi wake wa zamani.

Amesisitiza kuwa mchango wa kila mwana Tosa ni muhimu katika kufanikisha lengo hilo, akiwataka Alumni kutumia fursa hiyo kuunga mkono maendeleo ya shule yao na kuhakikisha wanafunzi waliopo sasa wanapata mazingira bora ya kusoma na kufanya vizuri kitaaluma.

Amesema lengo la mwisho ni kuona juhudi hizo zinasaidia kuboresha mazingira ya shule na kuwawezesha wanafunzi kusoma katika mazingira rafiki yatakayowapa nafasi kubwa ya kufaulu na kutimiza ndoto zao.





-AAHIDI KUFANYA KAZI KWA UADILIFU, UTII NA UZALENDO

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Deogratius Ndejembi, amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kumpa dhamana ya kuwa msaidizi namba moja na kuahidi utii, uadilifu, uzalendo na uchapaji kazi.

Makamu wa Rais amesema hayo, wakati akiwasalimu wananchi wa Jimbo la Chamwino, waliojitokeza kumpokea kwa wingi nje ya Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma, mara baada ya kuapishwa kuwa Makamu wa Rais. Amesema ataendelea kufanya kazi ya kumsaidia Mhe. Rais kwa uadilifu na kuwatumikia watanzania wote ili kuharakisha maendeleo.

Aidha Makamu wa Rais amesema ataendelea kuwawakilisha vyema vijana hapa nchini na kufanya kazi kwa bidii kuhakikisha Tanzania inazidi kusonga mbele katika nyanja mbalimbali za maendeleo.

Akitoa salamu zake kwa wananchi hao, Makamu wa Rais amewahakikishia kuendelea kutekeleza majukumu yake mapya kwa uadilifu, bidii na kwa kuzingatia maslahi mapana ya Taifa.

“Wana sitawazingua, na Mama sitamzingua,” amesema Ndejembi, katika ujumbe uliosisitiza dhamira yake ya kutekeleza wajibu aliopewa na kuendelea kuwa mwaminifu na mwakilishi mwema wa vijana.

Makamu wa Rais amewasalimu wananchi wa Jimbo la Chamwino ikiwa ni
jimbo alilolitumikia kabla ya kuteuliwa kuwa Makamu wa Rais.














Na TAEC Dodoma


Kila mwaka tarehe 29 Agosti, dunia huadhimisha Siku ya Kimataifa ya Kupinga Majaribio ya Nyuklia (International Day against Nuclear Tests), ikiwa ni fursa ya kutafakari madhara yaliyosababishwa na majaribio ya silaha za nyuklia na kuendelea kuhimiza juhudi za kujenga dunia yenye amani na usalama.

Siku hii ilianzishwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mwaka 2009 kupitia Azimio Na. 64/35, kwa lengo la kuongeza uelewa kuhusu madhara ya majaribio ya silaha za nyuklia na umuhimu wa kuyasitisha. Tarehe 29 Agosti pia ina umuhimu wa kihistoria kutokana na kufungwa kwa eneo la majaribio ya nyuklia la Semipalatinsk nchini Kazakhstan mwaka 1991.

Tangu jaribio la kwanza la silaha ya nyuklia mwaka 1945, zaidi ya majaribio 2,000 yamefanyika duniani, yakiacha historia ya madhara kwa afya ya binadamu, mazingira na usalama wa dunia.

Katika kuadhimisha siku hii, Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) inaungana na jumuiya ya kimataifa kupinga majaribio ya silaha za nyuklia na kusisitiza matumizi salama, yenye uwajibikaji na ya amani ya sayansi na teknolojia ya nyuklia.

Ni muhimu kuelewa kuwa kupinga majaribio ya silaha za nyuklia si kupinga teknolojia ya nyuklia. Teknolojia hii inapotumika kwa madhumuni ya amani na chini ya mifumo madhubuti ya usalama na udhibiti, ina mchango mkubwa katika kuboresha maisha na kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Nchini Tanzania, TAEC ina jukumu la kusimamia na kudhibiti matumizi salama ya vyanzo vya mionzi pamoja na kuhamasisha matumizi ya amani ya teknolojia ya nyuklia katika sekta mbalimbali zikiwemo afya, kilimo, mifugo, viwanda, migodi, maji, utafiti, mazingira na nishati.

Katika afya, teknolojia ya mionzi inatumika katika uchunguzi na matibabu ya magonjwa mbalimbali; katika kilimo na mifugo inachangia katika utafiti, uboreshaji wa uzalishaji na udhibiti wa baadhi ya wadudu na magonjwa. Mbinu za nyuklia pia zina matumizi muhimu katika tafiti za rasilimali za maji, viwanda, migodi na maeneo mengine ya maendeleo.

Kwa msingi huo, tunapaswa kutofautisha kati ya matumizi ya nyuklia kwa madhumuni ya kijeshi na matumizi yake kwa madhumuni ya amani. Hofu inayotokana na madhara ya silaha za nyuklia isiwe sababu ya kuiona teknolojia yote ya nyuklia kama tishio.

TAEC itaendelea kuhakikisha matumizi ya vyanzo vya mionzi nchini yanafanyika kwa kuzingatia sheria na viwango vya usalama ili kuwalinda wafanyakazi, wagonjwa, wananchi na mazingira. Tutaendelea pia kutoa elimu kwa umma ili kuondoa dhana potofu na kuongeza uelewa kuhusu manufaa ya matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia.

Tunapoadhimisha Siku ya Kimataifa ya Kupinga Majaribio ya Nyuklia, tunatoa wito kwa wananchi kuendelea kupata taarifa sahihi na kuunga mkono matumizi salama na ya amani ya teknolojia ya nyuklia kwa manufaa ya Taifa na ustawi wa binadamu.

Ujumbe wetu ni wazi: HAPANA kwa majaribio ya silaha za nyuklia; NDIYO kwa matumizi salama na ya amani ya teknolojia ya nyuklia kwa maendeleo ya Taifa.

“Mionzi kwa Matumizi Salama na Teknolojia ya Nyuklia kwa Maendeleo ya Taifa.”

Na Janeth Raphael - MichuziTv -Ikulu Chamwino 

 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema uamuzi wa kumteua Deogratius Ndejembi kuwa Makamu wa Rais ulizingatia sifa, uzoefu na uwezo wake wa kubeba dhamana kubwa ya uongozi wa taifa.

Rais Samia amesema nafasi hiyo imekabidhiwa tena kwa kijana, akimtaka Ndejembi kutumia fursa hiyo kujifunza, kukua kiakili na kutekeleza majukumu yake kwa weledi, utii na uaminifu kwa maslahi ya Watanzania.

Akizungumza leo, Agosti 29, 2026, katika hafla ya kumuapisha Ndejembi kuwa Makamu wa Rais iliyofanyika Ikulu Chamwino, Dodoma, Rais Samia amesema uamuzi wa kumrudisha kijana katika nafasi hiyo ulifanyika kwa kauli moja.

“Kwa kauli moja tuliamua kuirudisha nafasi ya Makamu wa Rais kwa vijana na tuendelee kulea. Imetoka kwa kijana na tumeirudisha kwa kijana. Tunakuomba kijana (Ndejembi) ukakue sio kwa umri bali ukakue kiakili, tumekupa majukumu makubwa ni imani yangu utaweza,” amesema Rais Samia.

Rais Samia amesema Ndejembi alipata uungwaji mkono wa wabunge kwa kauli moja kutokana na sifa alizonazo zinazomfanya astahili kushika nafasi hiyo.

“Wabunge walimpitisha Deogratius Ndejembi kwa kauli moja kwa kuzingatia sifa za Makamu wetu wa Rais,” amesema.

Amesema kabla ya kufikia nafasi ya Makamu wa Rais, Ndejembi amewahi kushika nafasi mbalimbali za uongozi serikalini na katika sekta binafsi, akieleza kuwa uzoefu huo utakuwa nyenzo muhimu katika utekelezaji wa majukumu yake mapya.

“Makamu wa Rais Deogratius Ndejembi, kabla ya wadhifa huu, ulishika nafasi mbalimbali za uongozi serikalini na sekta binafsi. Sina shaka kwamba uzoefu huo utakusaidia kutekeleza majukumu ya dhamana hii uliyopewa,” amesema Rais Samia.

Kwa mujibu wa Rais Samia, hakuna shule maalumu inayomwandaa mtu kuwa Makamu wa Rais, bali uwezo wa kutekeleza majukumu hayo unajengwa kupitia sifa binafsi, bidii, weledi, nidhamu pamoja na utayari wa kujifunza na kusimamia utekelezaji wa majukumu.

Amesema sifa hizo zitamsaidia Ndejembi kutekeleza ipasavyo dhamana aliyopewa na taifa.

Rais Samia pia amesema uzoefu wa Ndejembi ndio uliowafanya viongozi kutokuwa na kusita katika kupitisha jina lake wakati wa kutafuta mtu wa kujaza nafasi hiyo.

“Kwa uzoefu huo ndio maana wakati tunatafuta mtu wa kujaza nafasi hii, hatukusita hata kidogo kupitisha jina lako. Hivyo ni matamanio na matarajio yetu sote Watanzania utalitumikia vyema, kwa utii, uaminifu, utu, busara, uzalendo, hekima, maarifa na uzoefu ulio nao, ukimtanguliza Mungu mbele na kwa maslahi ya taifa,” amesema.

Katika hatua nyingine, Rais Samia amemtaka Ndejembi kwenda kuwatumikia Watanzania wote bila kujali tofauti zao, akisisitiza umuhimu wa kiongozi kuweka mbele maslahi ya taifa.

“Nenda ukawatumikie Watanzania bila kujali tofauti zao,” amesema Rais Samia.

Rais Samia amesema serikali ina kazi kubwa ya kutekeleza ahadi zilizowekwa kupitia Ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2025–2030, sambamba na kuanza utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya miaka 25 ijayo.

Amesema dira hiyo imebeba matarajio makubwa ya maendeleo kwa wananchi, hivyo utekelezaji wake unahitaji umoja, mshikamano, ushirikiano, utulivu na uongozi bora.

“Ili tuweze kutekeleza haya yote kwa maslahi ya wananchi wetu na taifa kwa ujumla, tunahitaji umoja, mshikamano, ushirikiano, utulivu na uongozi bora,” amesema.

Uapisho wa Ndejembi unafungua rasmi ukurasa mpya katika safari yake ya uongozi wa kitaifa, huku akianza kutekeleza majukumu ya Makamu wa Rais chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan


















 


Top News