Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) imemkaribisha rasmi Mkurugenzi Mtendaji mpya, CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi, katika ofisi za Makao Makuu ya Bodi hiyo jijini Dodoma, Aprili 1, 2026, ikiwa ni hatua ya kuanza rasmi kwa utekelezaji wa majukumu yake.
Akizungumza mara baada ya kuwasili ofisini hapo, CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi alisisitiza umuhimu wa ushirikiano kwa wafanyakazi, akibainisha kuwa mafanikio ya Taasisi yoyote yanategemea mshikamano, uwajibikaji na ufanisi wa kila mfanyakazi.
“Ni muhimu kila mmoja wetu akatimiza wajibu wake kwa ufanisi na kwa kuzingatia maadili ya kazi, ili kuendelea kujenga taswira nzuri ya Taasisi,” alisema CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi.
Aidha, alitumia fursa hiyo kusikiliza na kupokea kero pamoja na maoni mbalimbali kutoka kwa wafanyakazi, huku akiahidi kuyafanyia kazi kwa lengo la kuboresha mazingira ya utendaji kazi na kuongeza ufanisi ndani ya Taasisi.
Sambamba na hilo, CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi alikutana na Mhasibu Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, CPA Leonard Mkude, ofisini kwake jijini Dodoma, kwa lengo la kufahamiana na kuendeleza uhusiano wa kikazi uliopo kati ya ofisi hiyo na NBAA.
Katika mazungumzo yao, CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi alisisitiza dhamira ya kushirikiana kwa karibu na serikali pamoja na wadau wa Taaluma ya Uhasibu ili kuhakikisha Taaluma hiyo inaendelea kukua na kufikia viwango vya kimataifa.
“Tutashirikiana na Serikali na wadau mbalimbali wa Taaluma ya Uhasibu kuhakikisha kuwa Taaluma yetu inaendelea kuwa na viwango vya kimataifa, pamoja na kuimarisha uwazi na mawasiliano kwa wananchi,” alisema CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili katika ofisi za Makao Nakuu ya Bodi hiyo yaliyopo jijini Dodoma.
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi akizungumza jambo alipokuwa akitembelea ofisi za Bodi hiyo jijini Dodoma.
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi akizungumza na baadhi ya wafanyakazi wa NBAA alipowasili katika ofisi za Makao Makuu ya Bodi hiyo jijini Dodoma.
Baadhi ya wafanyakazi wa NBAA wakimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji wa NBAA, CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi alipokuwa akizungumza na wafanyakazi wa Bodi alipowasili katika ofisi za Makao Makuu ya Bodi hiyo jijini Dodoma.
Mhasibu Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, CPA Leonard Mkude akizungumza na Mkurugenzi Mtendaji mpya wa NBAA, CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi alipofika kujitambulisha katika ofisi yake jijini Dodoma akisindikizwa na baadhi ya viongozi wa NBAA.