Kiongozi amesema mabasi yanayoletwa katika soko la Tanzania yanapaswa kuzingatia mazingira ya barabara nchini, safari za masafa marefu, uimara, matumizi bora ya mafuta pamoja na kutoa huduma salama na yenye starehe kwa abiria.
Amesema usalama wa abiria unapaswa kupewa kipaumbele, huku akieleza kuwa ubora wa uhandisi, viwango vya usalama, teknolojia na muundo wa kisasa ni mambo muhimu kwa mabasi yanayolenga kuhudumia soko la Tanzania.
“Gharama za mafuta ni miongoni mwa gharama kubwa kwa kampuni za mabasi. Hivyo, basi lenye matumizi mazuri ya mafuta na utendaji mzuri linaweza kusaidia kupunguza gharama za uendeshaji na kuongeza ufanisi wa biashara,” amesema Kiongozi.
Aidha, ameitaka King Long kuwekeza katika huduma baada ya mauzo, ikiwemo vituo vya matengenezo, upatikanaji wa vipuri na wataalamu wa kiufundi nchini, huku akisisitiza umuhimu wa kampuni kusikiliza maoni na mahitaji ya wamiliki wa mabasi ili kuboresha huduma zake.
Kiongozi pia ameshauri kuanzishwa kwa mifumo rafiki ya upatikanaji wa fedha kwa wamiliki wa mabasi kwa kushirikiana na taasisi za fedha nchini, akisema si rahisi kwa waendeshaji wengi kulipa gharama yote ya basi kwa wakati mmoja. Amesema iwapo King Long itaunganisha ubora wa mabasi, dhamana, vipuri, huduma baada ya mauzo na uwezeshaji wa kifedha, itakuwa na nafasi ya kujenga uhusiano mzuri na waendeshaji wa usafirishaji nchini.
Kampuni ya usafirishaji ya Rasco imeeleza kuwa imekuwa ikitumia mabasi ya King Long tangu mwaka 2018, ikibainisha kuwa katika kipindi hicho imejionea ubora, uimara, starehe na ufanisi wa mabasi hayo katika huduma za usafirishaji.
Mwakilishi wa kampuni hiyo amesema kwa waendeshaji wa usafirishaji wa abiria, uchaguzi wa basi ni uamuzi muhimu unaozingatia ubora, usalama, uimara na uwezo wa gari kufanya kazi kwa ufanisi katika safari mbalimbali.
Amesema tangu waanze kutumia mabasi hayo, wameendelea kushuhudia maboresho yanayofanywa na King Long kupitia ubunifu na teknolojia ili kuendana na mahitaji ya sekta ya usafirishaji.
Ameongeza kuwa Rasco inajivunia kuhusishwa na chapa hiyo na kutambua mchango wake katika kukuza huduma za usafirishaji, hususan kwa kutoa mabasi yenye starehe na yanayokidhi mahitaji ya safari za masafa marefu.
Kwa mujibu wa mwakilishi huyo, uzoefu wa Rasco wa kutumia King Long kwa miaka kadhaa unaonyesha uimara na utendaji wa mabasi hayo, jambo linalowapa waendeshaji msingi wa kuzingatia ubora na ufanisi wanapofanya maamuzi ya ununuzi wa mabasi.
Amesema mabasi yanayotoa huduma bora, salama na yenye starehe yana umuhimu mkubwa katika kuhakikisha abiria wanafanya safari zao kwa usalama na faraja.
Kwa upande wake, Meneja Mauzo wa Kampuni ya King Long, Ally Bakari Mkali, amesema kampuni hiyo imejipanga kutoa huduma bora baada ya mauzo kwa wamiliki wa mabasi nchini Tanzania, ikiwamo msaada wa kitaalamu, matengenezo na upatikanaji wa vipuri halisi.
Akizungumza katika uzinduzi wa chapa hiyo nchini, Mkali amesema uhusiano na mteja hauishii katika ununuzi wa basi, bali unaendelea kupitia huduma za matengenezo na msaada wa kitaalamu. Amesema King Long inalenga kushirikiana na wataalamu wa ndani pamoja na wamiliki na waendeshaji wa mabasi ili kuhakikisha huduma na bidhaa zake zinaendana na mahitaji ya soko.
Amesema kampuni hiyo inalenga kuwa mshirika wa muda mrefu katika sekta ya usafirishaji Tanzania na Afrika Mashariki, kwa kutoa magari yenye uimara, usalama na faraja kwa wasafiri. Ameongeza kuwa mrejesho kutoka kwa wadau utasaidia kuboresha bidhaa na huduma, huku uzinduzi huo ukiwa mwanzo wa ushirikiano mpana zaidi katika soko la Tanzania.