Mkurugenzi wa TAWA TZ Engineering and Heaters Limited, Tawaqal Hassan, amesema kampuni hiyo imeshiriki Jukwaa la Tano la Utekelezaji wa Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini (LCCF 2026) linalofanyika jijini Mwanza kutokana na ubora wa bidhaa zake, hususan hita zinazotumika katika uchenjuaji wa madini. 

Akizungumza na waandishi wa habari Julai 22, 2026, alisema vifaa hivyo vina mchango mkubwa katika kuongeza ufanisi wa upatikanaji wa dhahabu wakati wa uchenjuaji wa madini, huku akieleza ubora wa hita zinazozalishwa na kampuni hiyo unapimwa kwa kuzingatia viwango, voltage inayozalishwa, pamoja na uimara wa bidhaa hizo na wamekuwa wakipokea maoni chanya kutoka kwa wateja na wadau wanaotumia bidhaa zao.

Kwa mujibu wa Hassan, TAWA TZ Engineering and Heaters Limited inajihusisha na utengenezaji wa hita kwa matumizi ya migodini, viwandani, mahoteli, Bekari, viwanda vinavyohitaji joto katika uzalishaji, pamoja na vifaa vya kuyeyusha lami, amesema bidhaa hizo zimetengenezwa kwa kuzingatia mahitaji ya soko na kutoa suluhisho la kudumu kwa watumiaji.

Aidha, amesema serikali imewawezesha wao Kama vijana kupitia utoaji wa vibali vya kutengeneza bidhaa hizo nchini, hatua ambayo imewapa fursa ya kuonyesha uwezo wao wa ubunifu na uzalishaji, ameongeza kuwa kampuni ipo tayari kuhudumia wateja wote wanaohitaji bidhaa hizo na inaendelea kujivunia kuwa miongoni mwa kampuni ya kwanza ya  Kitanzania kutengeneza hita za aina hiyo kwa viwango vya ubora.

Hassan amesema wateja wakuu wa kampuni hiyo ni sekta ya madini, huku akieleza kuwa ushiriki wao katika LCCF 2026 utawapa nafasi ya kujenga ushirikiano na wadau kutoka ndani na nje ya nchi, pia ametoa wito kwa Watanzania kuendelea kutumia bidhaa zinazozalishwa nchini ili kuunga mkono juhudi za wazawa, kukuza viwanda vya ndani na kuchochea maendeleo ya uchumi. 



Mwambata wa ubalozi  wa Oman nchini Tanzania, Abdulrahman Salim Algaad akiwa na familia yake, ametembelea Hifadhi ya Ngorongoro  na kushuhudia maajabu ya utalii yaliyopo katika kivutio namba moja cha utalii barani afrika

Akimpokea mwambata huyo, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi anayesimamia Huduma za Utalii na Masoko  Mariam  Kobelo ameeleza kuwa jitihada za mamlaka hiyo kuwafikia wadau mbalimbali zimeendelea kuzaa matunda ambapo watumishi kutoka balozi mbalimbali ndani na nje ya nchi wamendelea kutembelea hifadhi hiyo.

 Akiwa ndani ya hifadhi hiyo, Abdulrahman Algaad na familia yake walipata fursa ya kushuhudia wanyamapori adimu wakiwa katika mazingira yao ya asili, wanyamapori wakubwa watano, misitu, maporomoko ya maji, urithi wa utamaduni na mambo kale, makumbusho ya urithi geopark na kueleza kuwa ndoto na hisia alizokuwa nazo zimekutana na uhalisia.

 Mwambata huyo ameonyesha kuvutiwa na uzuri wa Hifadhi ya Ngorongoro na vivutio vya utalii vilivyopo Tanzania na kupongeza hatua za uhifadhi zinazofanyika na kuifanya Ngorongoro kuendelea kuheshimika kimataifa na kuwa eneo la urithi wa dunia lenye hadhi tatu za kimataifa.

 Kwa upande wake, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi anayesimamia huduma za utalii na masoko, Mariam Kobelo amebainisha kuwa ziara za viongozi na maafisa wa kidiplomasia wanaotembelea Ngorongoro zinachangia kuitangaza Tanzania kimataifa, kuimarisha ushirikiano katika sekta ya utalii, kuongeza ushirikiano kupitia diplomasia ya uchumi.






NA FARIDA MANGUBE MOROGOGO

Mradi wa kuongeza uwezo wa kusimamia Sera za Uchumi Jumuishi (IGE) umechangia Tanzania kuimarisha ukuaji wa uchumi, uundaji wa ajira na usimamizi endelevu wa mazingira kwa kuunganisha watafiti na watunga sera katika kutatua changamoto za maendeleo.

Mradi huo unaofadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Sweden (Sida) unatekelezwa katika Nchini za Tanzania, Uganda, Kenya, Rwanda na Ethiopia kwa lengo la kuimarisha sera za uchumi jumuishi zinazochochea maendeleo bila kuathiri mazingira.

Msimamizi Mkuu wa mradi huo nchini Tanzania kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dkt. Aloyce Hepelwa, amesema mradi umefanikiwa kuziba pengo lililokuwepo kati ya watafiti na watunga sera kwa kuwashirikisha katika kufanya tafiti na kuchambua changamoto zinazozuia ukuaji wa uchumi ili kupata suluhisho la pamoja.

Dkt. Hepelwa amesema kupitia Shule Kuu ya Uchumi ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, mradi unasaidia matumizi endelevu ya rasilimali za asili ikiwemo maji, misitu, madini na kilimo ili kuongeza tija ya uchumi huku ukilinda mazingira. Ameeleza kuwa ushirikiano huo umewezesha tafiti kutumika moja kwa moja katika kuboresha sera na maamuzi ya Serikali yanayolenga maendeleo endelevu.

Kwa upande wake, Mtafiti Mwandamizi kutoka Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Mhandisi Dkt. Befrina Igulu, amesema taasisi hiyo imekuwa ikishirikiana na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam katika kufanya tafiti zinazosaidia utekelezaji wa programu za uhifadhi wa mazingira na usimamizi wa rasilimali za asili kwa ufanisi zaidi.

Naye Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Usimamizi wa Mazingira katika Wizara ya Kilimo, Dkt. Rose Mbezi, amesema licha ya changamoto zinazosababishwa na mabadiliko ya tabianchi, sekta ya kilimo bado ni mhimili wa uchumi wa nchi nyingi za Afrika na pia imeendelea kutoa fursa mpya za maendeleo. Amesema takribani asilimia 70 ya Waafrika hutegemea kilimo kwa maisha yao, hivyo sera zinazochochea uchumi jumuishi na matumizi endelevu ya rasilimali ni muhimu katika kukuza uchumi na kuhimili athari za mabadiliko ya tabianchi.







Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, akiwasili katika ukumbi wa mikutano, jijini Accra, Ghana kwa ajili ya kushiriki Mkutano Maalum wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU) kuhusu Afya, tarehe 22 Julai, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Rais wa Jamhuri ya Ghana, Mhe. John Dramani Mahama, kabla ya ufunguzi wa Mkutano Maalum wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU) kuhusu Afya, unaofanyika jijini Accra, tarehe 22 Julai, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na viongozi mbalimbali kwenye Mkutano Maalum wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU) kuhusu Afya, jijini Accra, Ghana, tarehe 22 Julai, 2026.




 

Meneja Rasilimali Watu wa Mgodi wa Geita Gold Mining Limited (GGML), Dominick Marandu, amesema kampuni hiyo imeendelea kuwa kinara katika ushirikishwaji wa Watanzania kwenye sekta ya madini kupitia ajira, manunuzi na utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya jamii, amesema GGML imekuwa mshiriki na mdhamini wa Jukwaa la Utekelezaji wa Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini (LCCF) tangu lilipoanzishwa.

Akizungumza na waandishi wa habari Julai 22, 2026, wakati wa ufunguzi wa Jukwaa la Tano la LCCF jijini Mwanza, Marandu amesema kampuni hiyo inaamini rasilimali za madini zinapaswa kuwanufaisha Watanzania pamoja na jamii zinazozunguka maeneo ya migodi, amesisitiza kuwa ushirikishwaji wa wananchi ni sehemu muhimu ya maendeleo ya sekta hiyo.

Amesema GGML imefanikiwa kuwaajiri Watanzania kwa kiwango kikubwa, ambapo asilimia 98 ya wafanyakazi wake ni wazawa wenye taaluma na ujuzi mbalimbali wanaoshiriki katika shughuli za uzalishaji, na hatua hiyo inalenga kujenga uwezo wa wataalamu wa ndani na kuongeza mchango wao katika uchumi wa taifa.

Marandu pia ameeleza kuwa kampuni hiyo inaendelea kutoa kipaumbele kwa wazawa katika manunuzi, akibainisha kuwa asilimia 97 ya manunuzi yaliyofanyika katika nusu ya kwanza ya mwaka 2026 yalifanywa kupitia kampuni za Watanzania, ambapo GGML inafanya kazi kwa karibu na Tume ya Madini kuhakikisha sheria za maudhui ya ndani zinazingatiwa kikamilifu.

Aidha, kupitia programu ya Graduate, amesema zaidi ya wahitimu 300 wa vyuo vikuu wamenufaika katika kipindi cha miaka saba iliyopita kwa kupata mafunzo ya vitendo yanayowawezesha kupata uzoefu wa kazi, huku baadhi yao wakiajiriwa pindi nafasi zinapopatikana, aidha kampuni inaendelea kutekeleza takribani miradi 60 ya Uwajibikaji na urejeshaji kwa Jamii (CSR) katika maeneo yanayozunguka mgodi.

Marandu amewahimiza Watanzania, hususan vijana, kutumia fursa zinazotolewa na GGML kupitia ajira, mafunzo na utoaji wa huduma mbalimbali, amesema ushiriki wa wazawa katika sekta ya madini ni msingi wa kuongeza tija, kukuza uchumi na kuhakikisha rasilimali za nchi zinawanufaisha wananchi.



Na Benny Mwaipaja, London.


Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (MB), ameanza ziara ya kikazi ya siku sita jijini London, Uingereza, ambapo atashiriki katika matukio mbalimbali ikiwemo kuwa Mgeni Rasmi katika uzinduzi wa hatifungani ya kwanza ya nje yenye sarafu ya Shilingi ya Tanzania inayotolewa na Shirika la Fedha la Kimataila (IFC) katika Soko la Hisa la London

Hatifungani hiyo inatarajiwa kupanua fursa za uwekezaji nchini na kuvutia aina mpya za wawekezaji wa kimataifa ambao wataunga mkono ajenda ya maendeleo ya muda mrefu ya nchi.

Mhe. Balozi Omar alipowasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Heathrow, alilakiwa na Mwenyeji wake, Balozi wa Tanzania nchini Uingereza, Mhe. Balozi Mbelwa Kairuki, ambaye baadae Alasiri, alimkaribisha katika Ofisi za Ubalozi wa Tanzania Jijini London ambapo alipokea taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya Ubalozi na baadae kujadili ajenda za ziara hiyo.

Ziara ya Mheshimiwa Balozi Omar inayoanza leo tarehe 21 hadi 26 Julai 2026, inalenga kuimarisha ushiriki wa Tanzania katika masoko ya kimataifa ya fedha, kuvutia mitaji ya muda mrefu na kuithibitisha nchi kama moja ya maeneo yanayovutia zaidi uwekezaji barani Afrika.

Ziara hiyo pia inatoa fursa ya kufanya majadiliano na wasimamizi wa mali wa kimataifa, wawekezaji wa serikali, taasisi za uwekezaji wa maendeleo na benki za biashara kuhusu fursa zilizopo katika miundombinu, nishati, viwanda, kilimo, madini na huduma za kifedha.

Aidha, atashiriki mazungumzo ya pande mbili na washirika mbalimbali wa maendeleo na taasisi kubwa za kifedha duniani ikiwemo Benki ya Dunia, Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC), Standard Bank na Soko la Hisa la London, kuhusu mwelekeo wa uchumi wa nchi, Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 pamoja na Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Miaka Mitano (FYDP IV).














 


Serikali kupitia Sheria ya Madini Kifungu cha 9 imepiga marufuku raia wa kigeni kumiliki leseni ndogo za uchimbaji wa madini. 

Hatua hiyo inalenga kuhakikisha wazawa wanafaidika na rasilimali za madini zilizopo katika ardhi yao.

Waziri wa Madini, Mhe. Antony Mavunde amesema hayo wakati wa ziara ya kukagua miradi ya maendeleo Mkoa wa Geita, katika kata ya Igalula, Wilaya ya Nyang'hwale.

Amesema sheria hiyo inawalinda wazawa wanaohitaji maeneo ya kuchimba ili wanufaike na madini.

Hata hivyo Mavunde amefafanua kuwa kupitia Kifungu cha 3, raia wa kigeni anaweza kuingia katika leseni ndogo kama mshauri wa kiufundi wa mchimbaji mdogo. 

Katika utaratibu huo mpya, mwenye leseni atapata asilimia 30 tofauti na awali iliyokuwa chini.

Aidha Waziri amemuelekeza Afisa Madini Mkazi Mkoa wa Kimadini Mbogwe, Bw. Jeremia Hango kufuatilia leseni zote zisizofanyiwa utafiti kwa muda mrefu.

Amesema amefuta leseni 70 za utafiti mkubwa zikiwemo zile za Mkoa wa Kimadini Mbogwe, baada ya kubaini kuna maeneo yenye wamiliki lakini hayafanyiwi kazi.

Mavunde ameongeza kuwa leseni hizo zitagawiwa kwa Watanzania wote bila upendeleo wala kujuana na viongozi ili kila mmoja anufaike na rasilimali za madini.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhe. Martin Shigella amesisitiza leseni "bubu" zifutwe mara moja ili wananchi wapate maeneo ya uchimbaji.




Na Pamela Mollel Arusha,

Waandishi wa habari wametakiwa kuongeza matumizi ya ripoti za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) katika kuwapa wananchi taarifa sahihi kuhusu namna fedha na rasilimali za umma zinavyotumika nchini

Wito huo umetolewa na Mkaguzi wa Nje wa Mkoa wa Arusha, Valence Rutakyamirwa, wakati wa warsha maalumu iliyoandaliwa na Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi ya Tanzania (NAOT) kwa wanachama wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Arusha (APC)

Rutakyamirwa anasema ripoti za ukaguzi zina nafasi kubwa katika kuibua changamoto zilizopo kwenye usimamizi wa fedha za umma, utekelezaji wa miradi ya maendeleo na uzingatiaji wa sheria katika taasisi za serikali

Anasema jukumu la ukaguzi halilengi pekee kubaini makosa, bali pia kusaidia taasisi za umma kujenga mifumo bora ya usimamizi, kuongeza uwajibikaji na kuhakikisha wananchi wanapata huduma zinazostahili

“Waandishi wa habari wana nafasi muhimu ya kuzifanyia kazi ripoti hizi kwa kuzichambua, kufuatilia utekelezaji wa mapendekezo na kuelimisha jamii kuhusu matumizi ya fedha za umma,” anasema Rutakyamirwa.

Ameeleza kuwa katika kaguzi mbalimbali, NAOT imekuwa ikibaini changamoto katika maeneo ya manunuzi ya umma, usimamizi wa miradi ya maendeleo, utekelezaji wa mikataba na matumizi ya rasilimali za serikali

Kwa upande wake, Mchumi Mwandamizi kutoka Ofisi ya CAG, Emmanuel Lazaro, anasema taasisi hiyo inaendelea kuboresha mifumo yake ya ukaguzi kwa kutumia teknolojia za kisasa na mbinu mpya ili kuongeza ufanisi wa kazi

Anasema mpango mkakati wa NAOT unaendana na Dira ya Maendeleo ya Tanzania 2050 kwa kuzingatia kuimarisha uwajibikaji, utawala bora na mapambano dhidi ya vitendo vya rushwa

Aidha, Lazaro ametangaza mpango wa kuanzisha tuzo maalumu kwa waandishi wa habari watakaofanya kazi bora za uchunguzi zinazosaidia kuibua changamoto katika miradi ya maendeleo, matumizi ya fedha za umma na utekelezaji wa mapendekezo ya ukaguzi.

Hatua hiyo inalenga kuhamasisha uandishi wa habari unaochochea uwazi, uwajibikaji na usimamizi bora wa rasilimali za taifa.



Polisi kata na watendaji wa kata zilizopo Wilayani Mpanda Mkoani Katavi wametakiwa kuratibu na kufanya doria za kutosha kwa kushirikiana na vikundi vya ulinzi shirikishi ili kudumisha amani, utulivu na usalama uliyopo Kwenye kata zao. 

Wito huo umetolewa Julai 22, 2026 na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Katavi Kamishina Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Kaster Ngonyani katika kikao kazi kilicho wakutanisha Polisi Kata na watendaji wa kata zote zilizopo Wilayani Mpanda kilichofanyika Ukumbi wa Polisi Kantini Manispaa ya Mpanda.

Katika kikao hicho, kimewataka Polisi kata na watendaji kata kuhainisha maeneo korofi Kwenye kata zao na kuweka mikakati ya pamoja katika kufanya doria za kutosha kupitia vikundi vya ulinzi shirikishi pamoja na kutoa elimu kwa vikundi hivyo juu ya namna bora ya ufanyaji doria ikiwemo mbinu  matumizi ya nguvu za kadri na ukamataji salama bila kuleta madhara kwa wakamataji wa watuhumiwa wa uhalifu na kuwafikisha vituo .

Naye Mkuu wa Polisi Jamii Mkoa wa Katavi Mrakibu wa Polisi (SP) John Mwaipungu amewataka watendaji kata na Polisi kata hao kuendelea kutoa elimu mbalimbali kwa wananchi ikiwemo namna bora ya kukabiliana na matukio ya ukatili wa kijinsia pamoja na kudhibiti wizi kwa njia ya mitandao kwa kujenga tabia ya kupiga simu kabla ya kutuma pesa ili kuhakiki endapo namba wanazozitumia pesa wanazitambua. 

Aidha Mtendaji kata ya Ibindi Moses Mihayo amelipongeza Jeshi la Polisi kwa kuendelea kudumisha amani na utilivu inayoonekana katika maeneo yao pamoja na kuzidi kuwa karibu na wananchi kupitia Polisi kata na kuliomba Jeshi la Polisi kuendelea kufanya doria na misako ya mara kwa mara ili kutokomeza kabisa matukio ya kihalifu na wahalifu Kwenye makazi yao.









-Ufadhili wa dola milioni 100 waimarisha utekelezaji wa Agenda 2030 na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050

Benki ya NMB imewekeza takribani dola za Marekani milioni 100, sawa na Shilingi bilioni 224, katika mkopo wa pamoja wenye thamani ya dola milioni 500 kwa ajili ya Mgodi wa Dhahabu wa Geita, hatua inayoiweka kuwa benki kubwa zaidi kutoka Tanzania kushiriki katika ufadhili huo na kuimarisha mchango wake katika maendeleo ya sekta ya madini nchini.

Mkopo huo wa pamoja umeratibiwa na Nedbank Corporate and Investment Banking kwa ajili ya AngloGold Ashanti kupitia Mgodi wa Dhahabu wa Geita. Ushiriki wa Benki ya NMB unaonesha uwezo unaoongezeka wa taasisi za fedha za ndani kuhamasisha mtaji kwa ajili ya uwekezaji mkubwa wa kimkakati unaochochea ukuaji wa uchumi na maendeleo ya taifa.

Ufadhili huo unaendana na Agenda 2030 ya Benki ya NMB, ambayo imeitambua sekta ya madini kuwa miongoni mwa vichocheo muhimu vya ukuaji wa uchumi. Kupitia uwekezaji huo, benki inachangia kuimarisha mapato ya fedha za kigeni, minyororo ya thamani ya ndani, ajira, ununuzi wa bidhaa na huduma kutoka kwa wazabuni wa ndani pamoja na ushindani wa Tanzania katika uzalishaji na mauzo ya nje.

Hatua hiyo pia inaunga mkono Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, inayolenga kujenga uchumi wenye ushindani, unaojumuisha wananchi wengi zaidi, unaoongozwa na sekta binafsi na unaotegemea ukuaji wa viwanda, biashara na mauzo ya nje.

Mgodi wa Dhahabu wa Geita ni miongoni mwa miradi mikubwa ya madini nchini na wazalishaji wakubwa wa dhahabu barani Afrika. Ufadhili huo utawezesha kuendelea kwa uwekezaji katika mgodi huo na kusaidia kudumisha uzalishaji, mauzo ya nje, ajira, ununuzi wa ndani na thamani ya muda mrefu kwa uchumi wa Tanzania.

Akizungumzia hatua hiyo, Mkurugenzi  Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya NMB, Ruth Zaipuna, alisema muamala huo unaakisi mkakati wa benki wa kuelekeza mtaji katika sekta zenye uwezo mkubwa wa kuleta mageuzi katika uchumi wa Tanzania.

«“Muamala huu unaonesha uwezo wa Benki ya NMB kushiriki katika ufadhili mkubwa na wenye miundo ya kitaalamu sambamba na taasisi zinazoongoza za kifedha za kikanda na kimataifa, huku tukihakikisha mtaji wa Tanzania unakuwa sehemu muhimu ya uwekezaji wa kimkakati wa taifa. Huu ni utekelezaji wa Agenda 2030 kwa vitendo—kwa kutumia mtaji, utaalamu na ushirikiano wetu kuharakisha ukuaji endelevu wa uchumi na ustawi wa muda mrefu wa taifa.”»

Zaipuna alisema Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 imeweka mwelekeo wa kujenga uchumi wenye ushindani, unaojumuisha wote na unaoongozwa na viwanda, huku ufadhili wa uwekezaji wa kiwango hicho ukiimarisha sekta inayochangia mauzo ya nje, mapato ya fedha za kigeni, maendeleo ya biashara za ndani, ajira na mageuzi endelevu ya uchumi.

Hadi sasa, Benki ya NMB imeifadhili sekta ya madini kwa jumla ya takribani Shilingi bilioni 400, ikiunga mkono uchimbaji wenye uwajibikaji, ukuaji wa wazabuni wa ndani na uwekezaji katika mnyororo mzima wa thamani wa sekta hiyo.

Ushiriki wa benki katika ufadhili huo pia unaonesha uwezo unaoongezeka wa taasisi za fedha za Afrika kushirikiana katika miamala mikubwa na yenye miundo tata inayohamasisha mtaji wa muda mrefu kwa ajili ya uwekezaji wa kimkakati barani Afrika.

Benki ya NMB imeipongeza Nedbank Corporate  kwa kuratibu na kudhamini mkopo huo wa pamoja, ikisema muamala huo ni kielelezo cha nguvu ya ushirikiano wa taasisi za fedha za kikanda katika kuharakisha maendeleo endelevu ya uchumi wa Afrika. 


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na UN Women katika kukuza usawa wa kijinsia, kuwawezesha wanawake kiuchumi na kuzuia ukatili dhidi ya wanawake na wasichana.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 22 Julai 2026, Ikulu Zanzibar, alipokutana na Mwakilishi mpya wa UN Women nchini Tanzania, Bi. Julia Broussard, aliyefika kujitambulisha rasmi baada ya kuanza majukumu yake.

Katika mazungumzo hayo, Rais Dkt. Mwinyi amesisitiza kuimarishwa kwa ushirikiano katika maendeleo ya sekta ya mwani, matumizi ya takwimu za kijinsia, bajeti zinazozingatia usawa wa kijinsia na kuongeza ushiriki wa wanawake katika nafasi za uongozi.

Kwa upande wake, Bi. Julia Broussard ameipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa hatua zinazochukua katika kukuza usawa wa kijinsia na kuahidi kuwa UN Women itaendelea kushirikiana kwa karibu na Serikali katika kuwawezesha wanawake na kuboresha ustawi wa wanawake na wasichana Zanzibar. 













Top News