Manyara Tanzanite Marathon 2026, mbio za hisani zenye lengo la kuchangisha fedha kwa ajili ya ujenzi na uwezeshaji wa wodi maalum ya kuwahudumia watoto njiti, zimefanyika leo katika Mji wa Babati, zikiwa na kaulimbiu “Hatua Moja, Okoa Maisha ya Mtoto Njiti.”

Mbio hizo za hisani zimeongozwa na Mgeni Rasmi kwa niaba ya Waziri Mkuu, Mhe. Mwigulu Nchemba, Naibu Spika wa Bunge, Mhe. Daniel Sillo, ambaye amempongeza Mkuu wa Mkoa wa Manyara kwa ubunifu wa kuanzisha Manyara Tanzanite Marathon, akieleza kuwa mbio hizo ni sehemu ya jitihada za kuchangia moja kwa moja katika kuokoa maisha ya watoto njiti.

Manyara Tanzanite Marathon 2026 inalenga kukusanya jumla ya shilingi bilioni 1.5, fedha zitakazotumika katika ujenzi na uwezeshaji wa wodi maalum kwa ajili ya kutoa huduma kwa watoto wanaozaliwa kabla ya wakati.

Mbio hizo zimewakutanisha wananchi na wanariadha kutoka maeneo mbalimbali, katika kuunga mkono juhudi za kuboresha huduma za afya na kuokoa maisha ya watoto njiti.

Mbio za Hisani za Manyara Tanzanite Marathon zimefanyika leo mkoani Manyara, zikihudhuriwa na watu mbalimbali kutoka maeneo tofauti ya nchi pamoja na viongozi mbalimbali, huku lengo kuu likiwa ni kuchangisha fedha kwa ajili ya kuokoa maisha ya watoto wachanga na watoto njiti.
Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Daniel Sillo, aliyemwakilisha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye alitarajiwa kuwa mgeni rasmi katika mbio hizo, amepongeza uongozi wa Mkoa wa Manyara kwa ubunifu wa kuanzisha mbio hizo zinazolenga kuchangisha fedha kwa ajili ya kuimarisha huduma za afya na kuokoa maisha ya watoto wachanga na watoto njiti.

Sillo amesema hatua hiyo ni mfano wa ubunifu unaopaswa kuigwa na maeneo mengine nchini, akisisitiza umuhimu wa kushirikisha jamii na wadau katika kusaidia kuboresha huduma za afya.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa TAMISEMI, Jafari Rajabu, amesema mbio hizo zimeleta tija kubwa katika juhudi za kuokoa maisha ya watoto, akiwataka wananchi na wadau kuendelea kuunga mkono jitihada zinazolenga kuboresha afya ya watoto.

Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, amewashukuru wadau wote walioshiriki na kuunga mkono maandalizi ya mbio hizo, akisema ushiriki wao umewezesha kufanikisha azma ya kuchangisha fedha kwa ajili ya watoto wanaohitaji huduma maalumu za afya.

Baadhi ya washiriki wa mbio hizo wamesema, pamoja na kushiriki kwa ajili ya mazoezi na kuimarisha afya zao, wameona umuhimu wa kuwa sehemu ya harakati za kuchangia maisha ya watoto wachanga na watoto njiti.

Wamesema ushiriki wao katika Manyara Tanzanite Marathon umewapa fursa ya kufanya mazoezi huku wakitoa mchango wa moja kwa moja katika kusaidia kuokoa maisha ya watoto, hivyo kuwataka wananchi wengine kuendelea kushiriki katika matukio yenye malengo ya kijamii na kiafya.




































 

Na Mwandishi Wetu

TAKRIBANI wiki moja tangu agizo la kuondoa Stendi za Mabasi mitaani lianze kutekelezwa Jijini Dar es Salaam, wadau mbalimbali wamedai kushangazwa na hatua hiyo na kuiomba Serikali kurejesha huduma hiyo ili kuwaondolea usumbufu wananchi.

Wamesema hatua hiyo inatokana na ukweli kuwa wananchi wameanza 'kuonja joto la jiwe' kutokana na umbali kati ya mahali kilipo Kituo cha Mabasi cha Magufuli na maeneo watokapo hali inayowafanya wapate wakati mgumu. 

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na njia mbalimbali, pamoja na mambo mengine wadau hao wamesema hakuna kingine kitakachowaondolea adha hiyo wananchi zaidi ya busara za viongozi pamoja watoa huduma na kwamba kwa namna ilivyo inaonesha kama kuna hali ya kutaka kukomoana.

Mkazi wa Kigamboni ambaye pia ni Mwandishi wa vitabu na mgombea wa Ubunge wa Jimbo la Kigamboni katika Uchaguzi wa Oktoba Mwaka jana kupitia CHAUMA Yericko Nyerere, amesema kama lengo la Serikali ni kurahisisha maisha ya wananchi basi inaonesha kuwa haijashauriwa vizuri  kuviondoa vituo vya mabasi mitaani.

Kupitia andiko lake katika akaunti yake ya  mtandao wa kijamii wa Instagram, amesema ikiwa Jiji la Dar es Salaam lina Wilaya tano (5) tena zikiwa maeneo ya mbalimbali na zote zikiwa na idadi kubwa ya watu, haiwezekani kutolea mfano wa Kituo Cha 'SGR' Bandari au Airport ukasema ndiyo mfano wa Stendi ya mabasi kuwa sehemu moja.

Amesema Dar es Salaam inayokadiriwa kuwa na wakazi zaidi ya Milioni 7, wastani wa asilimia 84 ya wananchi wake hutegemea usafiri wa mabasi huku kwa siku ikikadiriwa kuwa takribani watu laki 2 wanaingia na kutoka kupitia usafiri huo Jijini humo hivyo ni ngumu wote kuwajaza sehemu moja.

"Kutoka Kata ya PembaMnazi, Wilaya ya Kigamboni hadi Stendi ya Magufuli ni kilomita 67, chukulia huyu mwananchi anataka kusafiri kwenda Mbeya huyu hawezi kutoka alfajiri akawahi basi pale Magufuli, atalazimika kusafiri siku moja kabla akalale Mbezi  Stendi ili asubuhi awahi basi na hii ni karbe ya 21 ya Sayansi na tekonolojia" amesema Nyerere.

Mdau mkubwa wa mitandao ya Kijamii Christopher Cyrilo,  ameenda mbali na kuhoji kuwa lipi lengo hasa la agizo hilo, je ni kuongeza mapato kwa Serikali kupitia stendi ya Magufuli au kuna sababu nyingine lakini kabla ya kuwatoa katika maeneo waliyokuwa wenye Mabasi hao walipata wapi vibali vya kutoa huduma maeneo hao.

" Je Ofisi hizo zilipata Usajili wa LATRA ? kama hazikujasiliwa Kuna adhabu  wamepewa na kama walisajiliwa je watalipwa fidia kwa usumbufu? " Amehoji Cyrilo kupitia andiko lake katika mtandao wa kijamii wa Facebook

Ameongeza kuwa endapo LATRA ilitoa Usajili alafu Mkuu wa Mkoa naye akatoa agizo lake kunaonesha kuna hali ya kutofautiana ndani Ofisi hizo mbili za Serikali huku akihoji ni faida zipi ambazo abiria wa mikoani wananufaika nazo kutokana na agizo hilo la Chalamila.

Amesisitiza kuwa anachoona yeye hatua ya wafanyabiashara wa mabasi kujenga Ofisi zao Shekilango, Chanika, Manzese, Magomeni, Kigamboni na kwingineko kulilenga kurahisisha huduma za usafiri kwa wateja wapo ili kuwaondolea hali ya usumbufu.  

Aidha  Chama Cha Wamiliki wa Mabasi nchini ( TABOA) kupitia kwa Katibu  wake Mkuu Priscus John Nimesema pamoja na agizo hilo wanachoiomba Serikali kuwaruhusu kwenda kushusha abiria wao katika maeneo mengine zilipo Ofisi zao mara baada ya kuingia na kushusha katika Kituo Cha Magufuli.

Amesema hawaoni tatizo kama mabasi yatapita Magufuli kushusha pamoja na kufanyiwa ukaguzi mbambali na taasisi za Serikali hususani Uhamiaji na zingine kIsha kwenda kushusha abiria maeneo mengine kwani kufanya hivyo pamoja na mambo mengine kutawaondolea Hali ya usumbufu abiria.

Hata hivyo wakati hayo yakiendelea kutokea imedaiwa kuwa zipo baadhi ya kampuni za Mabasi zimeamua kusitisha huduma zao za kusafirisha abiria na 'kupaki' mabasi yao kutokana na hali hiyo jambo lililopelekea baadhi ya watoa huduma wa Kampuni hizo kupata wakati mgumu kutokana na kukosa ajira.

Benki ya Absa Tanzania, kwa kushirikiana na GirlCode, shirika lisilo la kiserikali lenye makao yake nchini Afrika Kusini linalolenga kuwawezesha wasichana kutoka mazingira yenye changamoto kwa kuwapatia ujuzi na rasilimali za kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika sekta ya teknolojia, imetangaza kurejea kwa mashindano ya GirlCode Tanzania Hackathon kwa mwaka wa pili mfululizo.

Hatua hiyo inafuatia mafanikio makubwa yaliyopatikana mwaka 2025, ambapo timu ya Tanzania iliibuka na tuzo kuu ya Pan-African Grand Prize yenye thamani ya Dola za Marekani 5,000.

GirlCode Hackathon ni sehemu ya mpango mpana wa GirlCode unaolenga kuwawezesha wanawake vijana barani Afrika kwa kuwapatia ujuzi wa vitendo katika teknolojia, kuwaunganisha na walezi na wataalamu kupitia programu za ushauri, pamoja na kuwapa fursa ya kubuni suluhisho zinazolenga kukabiliana na changamoto halisi katika jamii zao.

Kurudi kwa mashindano hayo nchini Tanzania kunatajwa kuwa hatua muhimu katika kuimarisha kizazi cha wataalamu wanawake katika teknolojia na kujenga juu ya mafanikio yaliyopatikana na washiriki wa Tanzania mwaka jana.

Ushindi wa Tanzania mwaka 2025 ulidhihirisha umuhimu wa kuwekeza kwa wanawake vijana kama wabunifu, wajenzi wa suluhisho na watatuzi wa changamoto. Mafanikio hayo hayakuweka tu Tanzania katika ramani ya GirlCode Hackathon barani Afrika, bali pia yalitoa hamasa kwa wanawake vijana zaidi nchini kujiona kuwa sehemu ya uchumi wa kidijitali unaokua barani Afrika.

Akizungumzia kurejea kwa mpango huo nchini Tanzania, Ofisa Mtendaji Mkuu wa GirlCode, Zandile Mkwanazi, alisema shirika hilo linajivunia mafanikio yaliyopatikana na timu ya Tanzania mwaka jana.

“GirlCode inajivunia sana kile ambacho timu ya Tanzania ilifanikiwa kukipata mwaka jana. Kushinda tuzo kuu ya Pan-African Grand Prize kumeonyesha kiwango cha vipaji, ubunifu na uwezo uliopo miongoni mwa wanawake vijana nchini Tanzania,” alisema.

Aliongeza kuwa kurejea kwa mashindano hayo kwa mwaka wa pili kunalenga kujenga juu ya mafanikio yaliyopatikana na kuwapa wanawake vijana zaidi fursa ya kuendeleza ujuzi wao, kufanya kazi kwa pamoja na kubuni suluhisho zinazotumia teknolojia na ambazo zinaweza kuwa na matokeo chanya katika jamii.

Hackathon ya mwaka huu itawakutanisha wanafunzi wa kike, wahitimu, wanaotarajia kuwa watengenezaji wa programu pamoja na wabunifu vijana, ambao watashirikiana katika timu, kupata ushauri kutoka kwa wataalamu na kuwasilisha suluhisho zao mbele ya jopo la majaji.

Washiriki watatakiwa kutumia fikra tunduizi, kutumia ujuzi wao wa kiteknolojia na kubuni mawazo mapya yanayoweza kuchangia katika mustakabali wa ajira, ujasiriamali na mageuzi ya kidijitali.

Mbali na mashindano, mpango huo utatoa jukwaa muhimu kwa wanawake vijana kupata uzoefu na uelewa zaidi kuhusu sekta ya teknolojia, kuunganishwa na wenzao pamoja na washauri, na kujenga kujiamini katika kutafuta ajira na fursa mbalimbali katika sekta hiyo.

Kwa washiriki wengi, uzoefu huo unaweza kuwa hatua ya kuingia katika programu za mafunzo kwa vitendo, ajira, ujasiriamali na kuendelea kujifunza katika teknolojia.

Akizungumzia umuhimu wa mpango huo, Ofisa Mkuu wa Uendeshaji wa Benki ya Absa Tanzania, Oscar Mwamfwagasi, alisema ushiriki wa waanzilishi wa biashara ndogo na za kati (SMEs) ni moja ya mambo yanayoongeza thamani katika Hackathon ya mwaka huu.

“Kinachofanya Hackathon ya mwaka huu kuwa na thamani zaidi ni ushiriki wa moja kwa moja wa waanzilishi wa biashara ndogo na za kati, ambao wanaleta uzoefu wa vitendo katika biashara pamoja na changamoto halisi zinazokabili biashara kwenye programu hii.”

Alisema ushiriki wao unasaidia kuboresha safari ya kujifunza kwa washiriki, huku ukifungua fursa kwa kampuni changa kuonyesha mawazo yao, kupata mwongozo kutoka kwa wataalamu wa sekta mbalimbali na kujenga mahusiano yanayoweza kusaidia kuharakisha ukuaji wa biashara zao.

“Programu kama hii ni muhimu katika kukuza ubunifu, kuwawezesha wajasiriamali na kujenga mfumo jumuishi zaidi wa kidijitali unaosaidia maendeleo endelevu ya Afrika,” alisema Mwamfwagasi.

Kadiri GirlCode Hackathon inavyoendelea kukua katika mataifa mbalimbali ya Afrika, Tanzania imeendelea kuwa mfano wa kile kinachoweza kufikiwa pale wanawake vijana wanapopewa majukwaa, rasilimali na mitandao sahihi ya kuwawezesha.

Ushindi wa Tanzania katika mashindano ya Pan-African mwaka 2025 umeweka msingi imara, huku toleo la mwaka huu likilenga kutoa hamasa kwa kizazi kijacho cha wanawake wa Tanzania wanaotaka kujikita katika teknolojia kufikia mafanikio makubwa zaidi.

GirlCode imewahimiza wanawake vijana nchini Tanzania, wadau, walezi na washiriki wa mfumo wa teknolojia kuunga mkono Hackathon ya mwaka huu na kushirikiana katika kujenga mustakabali wa kidijitali unaojumuisha watu wengi zaidi barani Afrika.

GirlCode Tanzania Hackathon 2026 itafanyika tarehe 26–27 Septemba 2026.

Maombi ya ushiriki: https://www.girlcode.co.za/hackathon-2026



Na Julitha Mlay ,NATCOM
KATIBU Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo, ametembelea Banda la Tume ya Taifa ya UNESCO ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika maadhimisho ya Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu Kitaifa yanayoendelea jijini Tanga.

Katika ziara hiyo, Prof. Nombo alipata fursa ya kujionea shughuli mbalimbali zinazofanywa na Tume hiyo, pamoja na maudhui yanayotolewa kwa umma kuhusu UNESCO, majukumu ya Tume na programu zake katika maeneo ya elimu, sayansi, utamaduni, mawasiliano na taarifa.

Prof. Nombo aliambatana na Mkurugenzi wa Elimu ya Ufundi, Dkt. Fredrick Salukele, ambapo walipata maelezo kuhusu namna Tume inavyotumia majukwaa ya kitaifa kuwafikia wananchi, wanafunzi, walimu, vijana na wadau mbalimbali kwa kuwapatia taarifa kuhusu UNESCO na fursa zinazopatikana kupitia programu zake.

Ushiriki wa Tume ya Taifa ya UNESCO katika Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu Kitaifa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha uelewa wa umma kuhusu UNESCO, pamoja na kuonesha mchango wa elimu, sayansi, utamaduni, mawasiliano na taarifa katika kukuza maarifa, ubunifu na maendeleo endelevu nchini.

Kupitia maonesho hayo, Tume inaendelea kuwafikishia wananchi taarifa kuhusu kazi za UNESCO na maeneo mbalimbali yanayohusiana na utekelezaji wa programu zake nchini Tanzania, huku ikihamasisha jamii kutumia maarifa na fursa zilizopo kwa maendeleo ya mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.

Maadhimisho ya Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu Kitaifa yanaendelea jijini Tanga yakishirikisha taasisi na wadau mbalimbali wa sekta ya elimu, ujuzi na ubunifu, kwa lengo la kuelimisha jamii kuhusu fursa, huduma na jitihada zinazochangia maendeleo ya rasilimali watu nchini




MWANAFUNZI wa Kidato cha Tatu katika Shule ya Ufundi Tanga, Neema Bundala akionesha uwezo wake wa kujua mfumo wa nchini unafavyofanya kazi kwenye Banda la NACTVET ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea katika  katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara, jijini Tanga.

Na Mwandishi Wetu, Tanga
MWANAFUNZI wa Kidato cha Tatu katika Shule ya Ufundi Tanga, Neema Bundala, amesema mkondo wa Amali katika shule za sekondari unawajengea wanafunzi ujuzi unaowawezesha kujiajiri mara baada ya kumaliza masomo, huku wakisubiri matokeo ya mitihani ya Taifa.

Neema ameyasema hayo wakati akizungumza katika Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea katika Banda la Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET), katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara, jijini Tanga

Amesema anasoma fani ya Ufundi wa Magari (Motor Vehicle Mechanics), ambapo mafunzo hayo yanamwezesha kupata ujuzi wa vitendo utakaomsaidia kuanza kujiajiri mara baada ya kuhitimu.

“Kwa mfano mimi nasoma Ufundi wa Magari, hivyo ninapohitimu nitakuwa na ujuzi wa kutengeneza magari na ninaweza kuanza kujiajiri na nikisoma Kidato cha Tano na cha Sita, nitakuwa nimeongeza umahiri na nikifika chuo nitakuwa mbobezi zaidi,” amesema Neema.

Amesema mkondo wa Amali ni muhimu kwa wanafunzi wa kike kwa kuwa unawapa fursa ya kujenga uwezo wa kujiajiri na pia kuajirika katika taasisi mbalimbali kutokana na kuwa na ujuzi unaohitajika katika soko la ajira.
MWANAFUNZI wa Chuo cha VETA Tanga , Maria Moshi akizungumza na wananchi waliotembelea  Banda la VETA  kwenye  ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea katika  katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara, jijini Tanga waliotaka kujua mashine ya kutoteleshea vifaranga.


Na Mwandishi Wetu, Tanga
CHUO cha Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) Tanga kimebuni mashine ya kutotoleshea vifaranga yenye uwezo wa kutotolesha vifaranga 840 kwa wakati mmoja, huku mabaki ya maganda ya mayai yakitumika kutengeneza chakula cha kuku.

Akizungumza katika Banda la VETA kwenye Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara jijini Tanga, mwanafunzi wa chuo hicho, Maria Moshi, amesema mashine hiyo inatoa fursa kwa wafugaji na wajasiriamali kupata vifaranga bora na kuendeleza biashara ya kuku.

Amesema mashine hiyo inaambatana na mashine ya kupima na kuchambua mayai kabla ya kuingizwa kwenye mashine ya kutotoleshea, ambapo mayai yasiyofaa hutenganishwa.

Maria amesema mabaki ya maganda ya mayai yanaweza kuchanganywa na virutubisho na kusagwa ili kuzalisha chakula kingine kinachoweza kutumika katika ufugaji wa kuku.

“Kwa mtu anayefanya biashara ya kuku, mashine hii inampa uhakika wa kupata vifaranga vyenye ubora na baadaye kuwauza au kuendeleza ufugaji,” amesema Maria.

Amesema mashine ya kutotoleshea pamoja na mashine saidizi zinauzwa kwa Sh milioni tatu, huku Chuo kikiwa tayari kuzalisha mashine hizo kulingana na mahitaji ya wateja.
WAZIRI wa Uchukuzi Prof. Makame Mbarawa (Mb) akizungumza katika bamda la Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) alipotembelea wakati wa Kongamano la Nne la Kimataifa la Sekta ya Uchukuzi na Usafirishaji, linalofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam

Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) imepongezwa kwa kuendelea kusimamia sekta ya usafiri wa anga kwa ufanisi na kuimarisha utoaji wa huduma kupitia mifumo ya kisasa ya kidijitali.

Pongezi hizo zimetolewa na Waziri wa Uchukuzi Mh. Prof.Makame Mbarawa aliyekuwa mgeni rasmi katika Kongamano la Nne la Kimataifa la Sekta ya Uchukuzi na Usafirishaji, linalofanyika tarehe 20 na 21 Agosti 2026 katika Ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam ambalo TCAA imeshiriki, pindi alipotembelea banda la TCAA.

Mkuu wa Chuo cha Usafiri wa Anga Tanzania (CATC), Aristid Kanje akimuelezea Mhe. Waziri wa Uchukuzi Prof. Makame Mbarawa (Mb) alipotembelea wakati wa Kongamano la Nne la Kimataifa la Sekta ya Uchukuzi na Usafirishaji, linalofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam

Awali akiwa katika banda la TCAA, Prof. Mbarawa alipokewa na Mkuu wa Chuo cha Usafiri wa Anga Tanzania (CATC), Aristid Kanje, kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TCAA Dkt. Jabiri Bakari, ambaye alimweleza kuhusu shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na Mamlaka katika kusimamia na kuendeleza sekta ya usafiri wa anga nchini, ikiwemo matumizi ya teknolojia katika kuboresha utoaji wa huduma.

Kanje pia alimweleza Mh. Waziri kuhusu mfumo wa huduma za kielektroniki unaofahamika kama "Civil Aviation Services Portal (CASP)" unaowawezesha wadau wa usafiri wa anga kupata huduma kwa haraka na kwa ufanisi zaidi, pamoja na Dawati la Huduma kwa Wateja linalowezesha kupokea na kufuatilia maoni na changamoto za wadau.

Kongamano hilo limeandaliwa na Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) na limewakutanisha wadau kutoka sekta ya umma na binafsi kwa ajili ya kubadilishana uzoefu, maarifa na kujadili fursa na changamoto katika sekta ya uchukuzi na usafirishaji nchini.

Top News