




Na Mwandishi wetu.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), Bi. Khadija Ngasongwa, amefanya ziara ya kikazi katika Tume ya Ushindani Halali wa Biashara Zanzibar (ZFCC) ikiwa ni hatua ya kuimarisha mashirikiano kati ya taasisi hizo mbili katika masuala ya ushindani, ulinzi wa mlaji na udhibiti wa bidhaa bandia.
Bi. Ngasongwa alipokelewa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa ZFCC, Bi. Aliya Juma ambapo viongozi hao walifanya mazungumzo kuhusu kuendeleza ustawi wa taasisi hizo na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao.
Akizungumza katika ziara hiyo iliyofanyika tarehe 14 Januari, 2026 katika ofisi za ZFCC - Zanzibar, Bi. Ngasongwa alisema ushirikiano kati ya taasisi hizo unaendelea kuimarika kupitia utekelezaji wa Hati ya Makubaliano (MoU) yaliyokwisha sainiwa.
"FCC na ZFCC tayari zimeanza kutekeleza kwa vitendo maeneo ya ushirikiano ikiwemo kujengeana uwezo, kubadilishana uzoefu na kufanya ukaguzi wa pamoja ili kudhibiti bidhaa bandia na kulinda haki za watumiaji wa bidhaa au huduma."alisema Bi. Ngasongwa
Katika ziara hiyo, Bi. Ngasongwa pia alikutana na kuzungumza na menejimenti ya ZFCC ambapo walijadili namna ya kuendeleza mpango wa pamoja wa kuboresha mifumo ya utendaji kazi na kubadilishana taarifa.
Kikao hicho cha siku moja kilihitimishwa kwa pande zote mbili kuahidi kuendeleza juhudi za pamoja ili kuhakikisha mazingira ya biashara yanaendelea kuwa shindani, salama na rafiki kwa mlaji.

Katika mkutano huo uliofanyika katika Makao Makuu ya PSSSF jijini Dodoma, Mhe. Sangu amekumbusha kuwa kwa sasa Serikali inatekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo (DIRA 2025) ambayo, Pamoja na mambo mengine, inasisitiza uwekezaji katika miradi inayozalisha ajira na kuchochea Uchumi.
“Bodi ihakikishe mambo makubwa mawili katika utekelezaji wa miradi – kwanza kuzalisha ajira na pia ajira hizo ziwafikie vijana wa kitanzania kama DIRA 2050 na mipango ya Serikali inavyoelekeza,” amesema Waziri Sangu katika mkutano huo wake wa kwanza na Bodi ya Wadhamini ya PSSSF.
Katika mkutano huo, Menejimenti ya PSSSF nayo ilihudhuria ikiongozwa na Mkurugenzi Mkuu, Bw. Fortunatus Magambo.
Akizungumza katika mkutano huo, Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya PSSSF Bi. Joyce Mapunjo, kwa niaba ya Bodi, alimuhakikishia Waziri Sangu kuwa utekelezaji wa majukumu ya Mfuko unaongozwa na Mpango Mkakati uliohuishwa kwa kuzingatia DIRA 20250 na miongozo ya Serikali.
“Tumepokea maelekezo na tutazingatia katika utekelezaji … nikuhakikishie kuwa tuna Mpango Mkakati mpya (2026/2027 - 2030/2031) unaozingatia mipango ya kitaifa na pia tunatumia utaalam na uzoefu wetu kuhakikisha malengo ya Mfuko yanatimia na unaendelea kuwa stahimilivu,” amesema Bi. Mapunjo ambaye ni Katibu Mkuu mstaafu aliyehudumu kwenye Wizara mbalimbali.
Mfuko wa PSSSF ulianzishwa mwaka 2018 kufuatia kuunganishwa kwa iliyokuwa Mifuko ya GEPF, LAPF, PSPF na PPF. Kwa mujibu wa sheria iliyoanzisha Mfuko, PSSSF ina majukumu manne ya kusajili wanachama, kukusanya michango, kuwekeza ili kutunza thamani ya fedha na kulipa mafao mbalimbali kwa wanachama wake.

Kamati ya Usalama ya Wilaya ya Karatu, ikiongozwa na Mkuu wa Wilaya hiyo Mhe. Dkt. Lameck Karanga, imekutana na baadhi ya wananchi wa kabila la wahadzabe, kabila ambalo kwao nyama ya nyani ni kipaumbele kikubwa katika maisha yao na kukutana na wadatoga wanaojihusisha na uhunzi ,ziara ambayo imefanyika katika eneo la Eyasi wilayani humo.
Kabila la wahadzabe ambalo linaheshimika kutokana na mila na silka zake za kiasili linaamini kuwa nyama ya nyani ndiyo nyama bora na tamu kuliko zote duniani na limekuwa likimtumia mnyama huyo kama kielelezo muhimu kwa maisha yao huku kabila la wadatoga wakiendelea kutumia zana za kale katika uhunzi wa kufua bidhaa mbalimbali za kitamaduni.
Makabila yote mawili yanapatikana ndani ya jiopaki ya Ngorongoro Lengai inayopatikana wilaya ya Karatu, Ngorongoro na Monduli ,wilaya ambazo baadhi ya maeneo yake yanaunda jiopaki ya kidunia inayojulikana kama Ngorongoro Lengai Global Geopark inayotambuliwa na Shirika la Sayansi,Elimu na Utamaduni ( UNESCO).
Akizungumza na jamii ya makabila hayo Dkt. Lameck Karanga amewapongeza wananchi hao kwa kuendelea kutumisha mila na tamaduni za asili huku wakiwa kielelezo katika utunzaji wa amani na utulivu katika maeneo yao na kuwataka kuendelea kuwa kielelezo bora cha jamii nchini kwani serikali itaendelea kuwalinda na kuboresha shughuli za utalii katika eneo hilo.
Naibu Kamishna wa Uhifadhi, Utalii na Maendeleo ya jamii wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro bwana Joas Makwati ameeleza kuwa mradi wa Jiopaki ya Ngorongoro unanufaisha jamii zinazokaa ndani na nje ya eneo la Hifadhi ya Ngorongoro kwa kuwa Shughuli za ufugaji, uwindaji na kilimo hutegemea uwepo wa maji uhifadhi wa misitiu ya Ngorongoro.
Kabila la wahadzabe linaloishi pembezoni mwa eneo la Eyasi limekuwa likisifika kutokana na utaalam wake wa kuchoma na kula nyama za nyani jambo ambalo limewafanya wageni kutoka ndani nan je ya nchi kuwatembelea ili kuona jinsi mnyama huyo alivyokuwa tunu kwa kabila hilo.
Nyama ya nyani iliyochomwa vizuri kwa mujibu wa kabila hilo ina vionjo vitamu kutokana na mnyama huyo kula mizizi,matunda na mimea pori ambayo huifanya nyama yake kuwa na ladha ya kuvutia na yenye kuufanya mwili uweze kuhimili magonjwa mbalimbali.

Na. Emmanuel Buhohela, Dodoma
Kamati ya kudumu ya Bunge Ardhi, Maliasili na Utalii imeipongeza Serikali kwa kutatua kwa kiasi kikubwa changamoto ya upungufu wa Watumishi katika Taasisi zilizopo chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii.
Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Thimotheo Mzava Jijini Dodoma wakati kamati hiyo ikipewa mafunzo kuhusu Muundo na majukumu ya Wizara na Taasisi zake na kutaka jitihada hizo kuendelezwa ili kuwa na uwiano mzuri wa watumishi katika Taasisi ili ziweze kutekeleza kikamilifu majukumu yake.
Mhe. Mzava ameongeza kuwa kwa kipindi kilichopita kamati hiyo imekuwa ikipokea malalamiko ya upungufu wa watumishi tofauti na hali ilivyo sasa na kuiopongeza Serikali na kwamba Kamati hiyo ya kudumu ya Bunge inatarajia kuimarika kwa utendaji
Aidha, ameitaka wizara kuendekea kuvitazama na kuviwezesha vyuo vilivyoko chini ya wizara ili kuviwezesha kuzalisha wataalam na kutoa mchango katika sekta ya ajira.
Baadhi ya wajumbe wa Kamati hiyo waliopata fursa za kutoa ushauri na maelekezo wamesema wako tayari kushirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii katika kuendeleza uhifadhi ili kizazi kijacho kiweze kunufaika na rasilimali hiyo adhimu.
Akizungumza wakati wa kuhitimisha kikao cha leo Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji amesema Serikali inaendelea kuwa sikivu na kutekeleza majukumu yake ya kusimamia kikamilifu na kuendeleza sekta ya uhifadhi na Utalii ili kuwanufaisha wananchi wote.
Ameongeza kuwa kutokana na kauli mbiu ya chama cha mapinduzi ya kazi na utu Wizara itaendelea kutekeleza majukumu yake ipasavyo ili kufikia maono ya Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuacha tabasamu kwa wananchi pindi atakapomaliza muhula wake wa uongozi. Tanzania
Taasisi zilizowasikisha taarifa zake kwa niaba ya Mhe. Waziri wa Maliasili na Utalii ni Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI), Chuo Cha Usimamizi wa Wanyamapori (MWEKA) pamoja na Chuo Cha Taifa cha Utalii (NCT).
Kikao hicho kimeongozwa na mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Thimotheo Paul Mzava (Mb) na kuhudhuriwa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Hamad Hassan Chande (Mb.), Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt. Hassan Abbasi, Naibu Katibu Mkuu Bw. Nkoba Mabula, Menejimenti ya Wizara, Wakuu wa Taasisi pamoja na vyuo vilivyopo chini ya Wizara.
Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) mkoani Ruvuma limewahimiza wananchi na watumiaji wa umeme kuhakikisha wanalinda na kutunza miundombinu ya umeme iliyopo katika maeneo yao ili huduma ya umeme iendelee kupatikana kwa uhakika kama ilivyokusudiwa na Serikali.
Wito huo umetolewa na Afisa Uhusiano Huduma kwa Wateja wa TANESCO mkoani Ruvuma, Alan Njiro, wakati akitoa elimu kwa wananchi wa kijiji cha Selekano kilichopo katika kata ya Liganga, Halmashauri ya Wilaya ya Songea.
Akizungumza na wananchi hao ambao vitongoji vyao vimepitiwa na mradi wa REA, Njiro amewataka kushiriki kikamilifu katika utunzaji wa nguzo, nyaya na miundombinu mingine ya umeme ili kuepuka uharibifu unaoweza kusababisha kukatika kwa huduma ya umeme.
Aidha, amewasisitiza wananchi kuwa waangalifu katika malipo ya kuunganishiwa umeme, akieleza kuwa gharama ya kuunganishiwa umeme vijijini ni shilingi elfu ishirini na saba (27,000) tu, na kuwataka kuepuka kutoa fedha kwa watu kwani malipo yote hufanyika kupitia namba za kumbukumbu ya malipo.
Amesema TANESCO itaendelea kutoa elimu kwa wananchi ili kuhakikisha huduma ya umeme inalindwa na inawanufaisha wananchi katika kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Msafiri Mbibo, amekutana na uongozi wa Chama cha Mabroka wa Madini Tanzania (CHAMMATA) jijini Dodoma kwa lengo la kusikiliza na kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili mabroka wa madini nchini.
Kikao hicho kimehudhuriwa pia na Kamishna wa Madini, Dkt. Abdulrahman Mwanga, Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhani Lwamo, pamoja na watendaji wengine kutoka Wizara ya Madini na Tume ya Madini, hatua inayoonesha dhamira ya Serikali kushirikiana kwa karibu na wadau wa sekta ya madini katika kuendeleza sekta hiyo.
Akizungumza kwa niaba ya wanachama wa CHAMMATA, Mwenyekiti wa chama hicho, Jeremia Kituyo, amewasilisha changamoto mbalimbali zinazowakabili mabroka wa madini, ambapo mara baada ya kusikiliza hoja na maoni yaliyowasilishwa, Naibu Katibu Mkuu Mbibo amewahakikishia viongozi wa CHAMMATA kuwa Serikali itayafanyia kazi mapendekezo hayo kwa kushirikiana na taasisi husika, ili kuhakikisha changamoto hizo zinapatiwa ufumbuzi wa kudumu.
Mbibo amesisitiza kuwa Serikali kupitia Wizara ya Madini imeweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha wadau wote wa sekta ya madini, wakiwemo wachimbaji wadogo na wafanyabiashara wa madini, wanafanya kazi katika mazingira rafiki, salama na yenye tija kwa maendeleo ya sekta hiyo.
Ameongeza kuwa jitihada hizo zinalenga kuongeza uzalishaji, kuimarisha biashara ya madini kwa uwazi na ushindani, pamoja na kuhakikisha mchango wa sekta ya madini unaendelea kukua na kuchangia ipasavyo katika Pato la Taifa na maendeleo ya uchumi wa nchi kwa ujumla.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, wadau wa sekta ya madini wameipongeza Wizara ya Madini kwa kuchukua hatua kubwa za kuwawezesha wananchi, ikiwemo utoaji wa leseni za madini kwa vikundi vya vijana, kuwarasimisha wadau wa madini na kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za madini kwa mujibu wa sheria na kanuni za madini.
Aidha, wadau hao wameiomba Wizara ya Madini kuendelea kutoa msaada zaidi, hususan katika kuwaunganisha na Taasisi za Fedha ili kuwezesha upatikanaji wa mikopo itakayowaongezea uwezo wa mitaji na kuchochea ukuaji wa biashara zao za madini nchini.





.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)


.jpeg)

.jpeg)



.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)







