Na Farida Mangube, Morogoro
Jeshi la Polisi mkoani Morogoro limewakamata watuhumiwa watatu kwa tuhuma za kuhusika na matukio ya mauaji yaliyotokea katika wilaya za Malinyi, Kilombero na Kilosa.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro Kamishna msaidizi wa polisi ACP Andrew Gabriel Kantimbo amesema tukio la kwanza lilitokea katika kijiji cha Nyameni, kata ya Ulaya wilayani Kilosa, ambapo mwanamke aitwaye Janeth Ernest Mazengo (52) alifariki dunia baada ya kudaiwa kushambuliwa na mumewe, Amos Zakaria Kisomeko (64).
Inadaiwa kuwa chanzo cha tukio hilo ni wivu wa kimapenzi, ambapo mtuhumiwa alimshambulia marehemu kwa muda mrefu na kumsababishia majeraha makubwa yaliyosababisha kifo chake.
Katika tukio jingine lililotokea wilayani Kilombero ambapo Ramadhani Sadick Joseph (35) anashikiliwa kwa tuhuma za kumuua Messe Germanus Ngayungwa (23) mkazi wa Ifakara, marehemu alidaiwa kupigwa na kitu kizito hadi kupoteza maisha, huku chanzo kikitajwa kuwa ni mgogoro wa kifamilia.
Jeshi la Polisi limeeleza kuwa upelelezi wa matukio hayo unaendelea, na watuhumiwa watafikishwa mahakamani mara uchunguzi utakapokamilika.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Morogoro ametoa wito kwa wananchi kuacha kujichukulia sheria mkononi na badala yake kufuata taratibu za kisheria pale wanapokumbana na migogoro, ili kuepuka matukio ya ukatili yanayoweza kusababisha vifo.

Na Oscar Assenga
Kampuni ya Taifa Gesi imeendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa matumizi ya nishati safi, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuunga mkono sera ya Serikali ya kuhamasisha matumizi ya nishati rafiki kwa mazingira.
Akizungumza katika tamasha lililofanyika wilayani Handeni, Mkurugenzi wa Masoko wa Taifa Gesi, Oscar Shelukindo, alisema kampuni hiyo imekuwa ikishiriki katika matamasha ya kijamii tangu mwaka jana kwa lengo la kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi sahihi ya gesi safi.
Alisema kuwa katika tamasha hilo, wameelekeza nguvu zaidi kwa wakazi wa Handeni, hususan Kata ya Mdoe, ili kuwafikia wananchi wengi zaidi na kuwapa uelewa sahihi kuhusu faida za kutumia nishati hiyo.
“Tunafurahi kuwa hapa leo kutoa elimu ya matumizi ya gesi safi, kuondoa hofu kwa wananchi na kuwahamasisha kuachana na matumizi ya nishati zisizo rafiki kwa mazingira. Pia tunatoa gesi kwa bei nafuu ili kuwavutia zaidi kuitumia,” alisema Shelukindo.
Alifafanua kuwa bado kuna wananchi wengi ambao wana hofu au uelewa mdogo kuhusu matumizi ya gesi ya kupikia, hali inayowafanya kuendelea kutumia nishati kama kuni na mkaa, ambazo si rafiki kwa mazingira na pia zina madhara kiafya.
Kwa mujibu wa Shelukindo, utoaji wa elimu hiyo unalenga kubadili mtazamo wa jamii na kuwasaidia wananchi kuelewa kuwa gesi ni salama, nafuu kwa muda mrefu na rahisi kutumia.
Aidha, alisisitiza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mchango wa sekta binafsi katika kusaidia juhudi za Serikali za kulinda mazingira, kupunguza ukataji wa miti na kuboresha afya za wananchi kupitia matumizi ya nishati safi.
Wananchi waliohudhuria tamasha hilo walipata fursa ya kuuliza maswali, kujifunza matumizi sahihi ya gesi pamoja na kununua bidhaa za gesi kwa bei iliyopunguzwa.
Kwa ujumla, jitihada za Taifa Gesi zinaonesha namna sekta binafsi inavyoweza kushirikiana na Serikali katika kuhamasisha matumizi ya nishati safi, hatua inayotarajiwa kuleta mabadiliko chanya katika jamii, hususan maeneo ya vijijini.
Mkutano huo umepangwa kufanyika Aprili 11, 2026 katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na vyombo vya habari leo Jumamosi Aprili 4,2026 jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Wauzaji Chakula nchini kupitia Umoja wa Mamalishe na Babalishe Tanzania (UMALITA), Avijawa Omari, amesema kuwa wanaiomba Serikali kuwatambua rasmi kama kundi muhimu katika uchumi wa nchi.
Amesema kuwa utambuzi huo utawawezesha wanachama kupata mikopo, fursa za kiuchumi na kukuza ajira kwa vijana na wanawake nchini.
“Tunaomba Serikali ituone rasmi. Utambuzi utarahisisha upatikanaji wa mikopo na kutupa nafasi ya kupanua biashara zetu ili tuzalishe ajira zaidi,” amesema.
Bi Omari ameongeza kuwa mkutano huo utakuwa jukwaa muhimu kwa mamalishe na babalishe kuwasilisha moja kwa moja changamoto zao kwa viongozi wa Serikali kwa lengo la kuongeza kipato, kupanua biashara na kuchangia ukuaji wa ajira nchini.
Aidha, amewataka wanachama na wauzaji chakula wote nchini kujitokeza kwa wingi Aprili 11 katika ukumbi wa JNICC ili kujenga kwa pamoja mustakabali wa biashara zao.
Mkutano huo utafanyika chini ya kaulimbiu “Pika Kishua, Vaa Kishua” (Cook Smart, Dress Smart), inayolenga kuboresha viwango vya utoaji huduma na kuimarisha taswira ya kitaalamu ya wauzaji chakula nchini.
“Sisi ni wajasiriamali tunaojitegemea, na tunalisha taifa asubuhi, mchana, jioni hadi usiku. Tunaomba jamii itambue mchango wetu na kuheshimu kazi tunayoifanya,” aliongeza.
Ameeleza pia kuwa sekta hiyo imekuwa ikikabiliwa na changamoto mbalimbali, ikiwemo hatari za kiafya na mazingira magumu ya kazi, lakini sasa wameanza kuelekea katika matumizi ya nishati safi na mbinu bora za upishi ili kulinda afya na kukuza biashara.
Kwa upande wake, mwakilishi wa Babalishe, Ndugu Ngosha, amesisitiza umuhimu wa umoja na ushirikiano miongoni mwa wanachama ili kufikia malengo yao ya kiuchumi na kijamii.
Mkutano huo unatarajiwa kuwa wa kihistoria kwa kuwaunganisha wadau wakuu wa sekta isiyo rasmi na viongozi wa juu wa Serikali kujadili mustakabali wa ajira na ujasiriamali nchini.
.jpeg)

Nchi 26 Duniani kesho Aprili 5,2026 zinatarajia kuingia katika kinyang'anyiro cha mashindano ya kusoma quran yanayotarajiwa kufanyika Tanzania katika Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam.
Kufuatia mashindano hayo leo April 4,2026 Mufti Mkuu wa Tanzania Shekhe Abubakari Zuberi na jopo la kamati ya maandalizi wamepokea ugeni mkubwa kutoka Saudi Arabia kumpokea Imamu Mkuu wa Msikiti Mtakatifu wa Makka, Imamu Badri Al Turki.
Akizungumza na vyombo vya habari Imamu Mkuu wa Msikiti wa Makka Badri amesema amefurahi kufika nchi ya Tanzania inaonesha jinsi nchi za Afrika hasa Tanzania inavyopenda amani na kuendeleza Maendeleo ya dini kwa ujumla.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Jukwaa la Maimamu Tanzania(JUMADA) Imamu Suleiman Abdallah ametoa wito kwa Waislamu kote nchini kutumia fursa hiyo adhimu kumpokea mgeni huyo kuhudhuria katika mashindano hayo ikiwa na pamoja na kupata maombi ya imamu mkubwa duniani.
"Tukiwa kama Maimamu tumefurahi sana ujio Imamu Mkuu wa msikiti wa Makka sisi tutaitumia kama fursa" amesema Suleiman
By Hamis Shimye
Rais Dk. Samia Suluhu Hassan ameonyesha ni mwanasiasa wa kidemokrasia mwenye kufuata taratibu za demokrasia kwa dhamira yake ya muhimu ya kukutana na wagombea wa urais walioshiriki Uchaguzi Mkuu wa 2025 kutoka vyama vya upinzani Ikulu, jijini Dar es Salaam Machi 31, 2026.
Tukio hilo limefanyika katika mazingira ya ushirikiano na uwazi wa kisiasa, huku likilenga kuimarisha ushirikiano kati ya vyama vya siasa na utulivu wa taifa.
Katika mazungumzo hayo, wagombea wa upinzani walipewa fursa ya kuwasilisha maoni na hoja zao, na Rais Samia akajibu kwa uwazi, akisisitiza umuhimu wa uwajibikaji, heshima kwa sheria, na haki za raia.
Hatua hii ni ishara kwamba demokrasia nchini Tanzania inaendelea kukua kwa misingi ya ustaarabu na maadili ya kisiasa. Pia, imetoa tafsiri pana kuwa uongozi unaojumuisha pande zote ni chachu ya imani ya wananchi katika mfumo wa kidemokrasia.
Aidha, hatua hii inaonyesha wazi juu ya uongozi wa kiuwajibikaji na heshima kwa jamii aliyokuwa nayo Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuwatumikia Watanzania kwa ufanisi na uweledi mkubwa.
Kikao cha Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na viongozi wa upinzani kimeonyesha mfano wa ushirikiano kwa wagombea wote katika mchakato wa kisiasa na kuthibitisha kwamba uongozi wake unajali usawa, haki, na ustaarabu wa kisiasa ambao ni asili ya Tanzania.
Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amekuwa mstari wa mbele katika kufuata taratibu za kidemokrasia kwa kushirikisha wadau wa kisiasa, ikiwemo upinzani. Ameonyesha uwajibikaji na ustaarabu katika maamuzi ya kisiasa.
Kwa maneno mengine, siasa kwake sio tu uongozi wa serikali, bali pia ni mtindo wa kuunganisha mshikamano, maendeleo, na amani ya kisiasa huku akisukumwa na falsafa zake nne ambazo ni Maridhiano, Ustahamilivu, Mageuzi, na Kujenga upya.
Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amejitambulisha kama mwanasiasa wa kidemokrasia, ambaye anaamini kwa dhati katika ujenzi na ustawi wa taifa bora kupitia maridhiano na mshikamano wa kitaifa.
Uongozi wake umeendelea kuongozwa na imani kwamba maendeleo endelevu yanapatikana kwa kushirikisha wadau wote wa kisiasa, ikiwemo vyama vya upinzani, na kwa kuzingatia uwajibikaji, uwazi, na ustaarabu katika maamuzi ya serikali.
Mtazamo huo wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan unathibitisha kwamba siasa za kidemokrasia haziishii tu katika taratibu za kisheria, bali ni mtindo wa kuunganisha wananchi, kuendeleza mshikamano wa kitaifa, na kufanikisha maendeleo ya taifa.
Rais Samia anaendelea kuonyesha mfano wa kiongozi anayejali maridhiano, ustawi wa taifa, na maendeleo ya kila mwananchi, akithibitisha kuwa siasa za kidemokrasia ni msingi wa amani na maendeleo endelevu.
Hii inatokana na mfumo wa siasa zake hazishughulishi tu uongozi wa serikali, bali ni mtindo wa kuunganisha mshikamano, maendeleo, na amani ya kisiasa yenye kuonyesha maridhiano ya kweli ndio chachu ya amani na maendeleo.
Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anaendelea kuwa kielelezo cha uongozi wa kidemokrasia, akionyesha kwa vitendo siasa zenye uwajibikaji, ushirikishwaji na ustaarabu zinaweza kuendesha taifa kwa amani na maendeleo endelevu.
Kikao cha Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na viongozi wa upinzani kimeonyesha ushirikiano wa vyama vyote uliopo Tanzania na imeonyesha kwamba serikali haiji kwa nguvu pekee, bali inashirikisha upinzani katika maamuzi muhimu ya kitaifa.
Pia, kikao hicho kinakwenda kupunguza mvutano au mkwamo wa kisiasa na kimekuwa sehemu ya juhudi binafsi za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuondosha migongano ya kisiasa na kuleta maridhiano, utulivu wa kisiasa.
Kikao hicho ni ishara ya uimarishaji wa imani ya wananchi na kuwapa heshima viongozi wa upinzani jambo linaloongeza kuaminiana kati ya serikali, wananchi na vyama vya upinzani.
Huu ni mwendelezo wa ustaarabu wa kisiasa nchini Tanzania. Tukio hili linatuma ujumbe kwamba mazungumzo na kuheshimiana ni sehemu ya utawala na asili ya utamaduni wa Taifa la Tanzania.
Kuonyesha mtazamo wa kidemokrasia ambao unatoa ishara kwamba viongozi wanaweza kushirikiana bila kuchukua upande au kuchukiana bila sababu za msingi kwa kuwa taifa lina usawa wa kisiasa.
Hivyo, tukio hili lina tafsiri ya ushirikiano wa kweli, uwazi, na siasa za kidemokrasia zilizojengwa na waasisi wetu akiwemo Hayati Julius Nyerere na Sheikh Abeid Amaan Karume. Hongera viongozi na wagombea wa Urais kutoka vyama 16 vya siasa nchini vilivyoshiriki Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.
Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma
Serikali imelenga kuimarisha uwazi, uwajibikaji na ufanisi katika matumizi ya rasilimali za umma, sambamba na kuhakikisha upatikanaji wa bidhaa, huduma na kazi za ujenzi unazingatia ubora unaotakiwa, kwa wakati na kwa thamani halisi ya fedha (Value for Money).
Hayo yameelezwa na Kaimu Kamishina wa Idara ya Sera za Ununuzi wa Umma kutoka Wizara ya Fedha, Alex Haraba, wakati akitoa taarifa kwa umma kuelekea uzinduzi wa Sera ya Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya mwaka 2025.
Uzinduzi huo unatarajiwa kufanyika Aprili 8, 2026 katika Ukumbi wa Jakaya Kikwete, jijini Dodoma, ambapo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi.
Akizungumzia umuhimu wa sera hiyo, Haraba amesema ni hatua ya kimkakati inayolenga kuimarisha usimamizi wa rasilimali za umma pamoja na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa shughuli za Serikali kupitia mnyororo wa ugavi.
Amefafanua kuwa sera hiyo inalenga kufungamanisha shughuli zote za mnyororo wa ugavi ili kuimarisha utaratibu na usimamizi jumuishi, kuboresha matumizi ya rasilimali za umma, na kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa majukumu ya Serikali.
Kwa mujibu wa Haraba, kwa muda mrefu shughuli za mnyororo wa ugavi zimekuwa zikitekelezwa kupitia sheria, kanuni na mifumo mbalimbali bila kuwepo kwa mwongozo mmoja wa kisera unaounganisha hatua zote kwa mtazamo jumuishi.
Amesisitiza kuwa kutokana na sehemu kubwa ya matumizi ya Serikali kupita katika ununuzi wa umma, mnyororo wa ugavi ni nyenzo muhimu katika kuhakikisha rasilimali za umma zinasimamiwa kwa uwazi, ufanisi na uwajibikaji, hali itakayochochea ukuaji wa uchumi na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.
Aidha, sera hiyo inaweka mkazo katika kuimarisha utawala bora, matumizi ya teknolojia katika usimamizi wa mnyororo wa ugavi, pamoja na kuongeza ushiriki wa sekta binafsi na makundi maalum ya kijamii. Hatua hii inalenga kupanua fursa za kiuchumi na ajira kwa Watanzania, pamoja na kuhamasisha matumizi ya rasilimali na malighafi za ndani ili kuongeza thamani katika uzalishaji wa bidhaa na huduma.
Haraba ameongeza kuwa sera hiyo imeandaliwa kuweka mfumo jumuishi wa kimkakati wa kusimamia shughuli zote za mnyororo wa ugavi katika sekta ya umma. Mfumo huo unahusisha hatua mbalimbali kuanzia upangaji wa mahitaji, ununuzi wa umma, ugomboaji na uondoshaji wa mizigo ya Serikali, upokeaji na ukaguzi wa bidhaa, uhifadhi, matumizi na usambazaji, hadi uondoshaji wa mali za umma.
Uzinduzi wa sera hiyo unatarajiwa kuwa chachu ya maboresho makubwa katika usimamizi wa rasilimali za umma na kuongeza tija katika utoaji wa huduma za Serikali.
.png)
OWM-TAMISEMI
Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM– TAMISEMI) anayeshughulikia masuala ya Afya, Mhe. Dkt. Jafari Seif, amesema kuwa hali ya upatikanaji wa bidhaa za afya katika ngazi ya huduma za afya ya msingi nchini imeendelea kuimarika na kufikia kiwango cha kuridhisha ikilinganishwa na miaka iliyopita.
Akizungumza Aprili 2, 2026 jijini Dar es Salaam, katika kikao kazi kilichoongozwa na Waziri wa Afya, Mhe.Mohamed Mchengerwa, pamoja na wadau wa sekta ya afya, katika ofisi za Bohari ya Dawa (MSD), Mhe. Dkt. Seif amesema kuwa tathmini ya mwaka 2026 inaonesha hali ya upatikanaji wa dawa imefikia asilimia 89 katika hospitali, asilimia 88 katika vituo vya afya, na asilimia 88 katika zahanati.
Ameongeza kuwa katika mwaka wa fedha 2024/25, vituo vya kutolea huduma za afya ngazi ya msingi vilikusanya takribani Shilingi Bilioni 108, huku makusanyo hayo yakitarajiwa kuongezeka hadi kufikia Shilingi Bilioni 192 katika mwaka 2025/26.
Kwa upande wake, Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amemuelekeza Katibu Mkuu wa wizara hiyo kushirikiana kwa karibu na Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI kuandaa na kusimamia miongozo, taratibu na miundo ya usimamizi wa vituo vya kutolea huduma za afya. Lengo la hatua hiyo ni kuhakikisha kuwa wafamasia kote nchini wanakuwa sehemu muhimu ya timu za menejimenti katika vituo hivyo, ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za afya.
Na Benny Mwaipaja, Tangier-Morocco
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar, ametoa wito kwa nchi za Afrika kuwa na mtazamo wa pamoja katika kubuni na kutekeleza mikakati ya muda mfupi, wa kati na mrefu, ambayo ni endelevu na jumuishi, itakayopunguza utegemezi na kuimarisha uthabiti wa uchumi wa Bara la Afrika ili kukabiliana na majanga na migogoro ya vita inayoendelea duniani.
Mhe. Balozi Omar alitoa wito huo jijini Tangier nchini Morocco, katika Mkutano wa 58 wa Mawaziri wa Fedha, Mipango na Maendeleo ya Uchumi na Magavana wa Benki Kuu wa Afrika, wakati akichangia mjadala kufuatia taarifa ya Kamisheni ya Umoja wa Mataifa inayosimamia Uchumi Afrika (UNECA), inayochambua athari za mgogoro unaoendelea Mashariki ya Kati namna ulivyoleta athari hasi za kiuchumi na kijamii katika Bara la Afrika.
Alibainisha kuwa baadhi ya nchi za Afrika, hususan zile zinazotegemea sekta ya utalii, zinaweza kuathirika zaidi na Mgogoro unaoendelea Mashariki ya Kati.
Kwa upande wa Tanzania, alibainisha kuwa Serikali inaendelea kufuatilia kwa karibu mwenendo wa mgogoro huo kupitia ushirikiano katika Wizara za Kisekta na Taasisi zake, ili kubaini hatua stahiki za kisera zitakazolinda ustawi wa uchumi na maslahi ya wananchi.
Vilivile, alieleza kuwa pamoja na kwamba mgogoro huo umeathiri mtiririko wa biashara kwa kuwa ukanda wa Mashariki ya Kati ni lango muhimu la biashara kati ya Afrika na masoko ya kimataifa. Hivyo, ni muda muafaka wa Afrika kuona umuhimu wa kuwa na njia mbadala ya kufanya biashara hususan miongoni mwa nchi wanachama.
Mheshimiwa Balozi Omar alisisitiza kuwa kwa muda mrefu Afrika imekuwa ikijadili umuhimu wa kutumia rasilimali zake ipasavyo, na kwamba hali ya sasa inatoa fursa ya kuchukua hatua madhubuti za kujitegemea kwa kutumia rasilimali zake.
Alifafanua kuwa Bara la Afrika lina rasilimali za kutosha, ikiwemo mafuta na mbolea, ambazo zinaweza kuzalishwa na kupatikana ndani ya Bara kupitia ushirikiano, hususan Eneo Huru la Biashara Barani Afrika (AfCFTA).
Mhe. Balozi Omar alieleza kuhusu umuhimu wa kuendelea na majadiliano chini ya uratibu wa UNECA kuhusu mageuzi katika mifumo inayosimamia maamuzi na sera za kifedha duniani (Global Financial Architecture), ili Afrika iweze kuwa na sauti moja yenye nguvu katika upatikanaji wa rasilimali za kifedha kwa gharama nafuu kwa ajili ya maendeleo endelevu.
Alisisitiza kuwa mafanikio ya mageuzi hayo yatategemea mshikamano na ushirikiano thabiti wa nchi za Afrika.
Baadhi ya Washiriki wa Mkutano huo, walieleza kuwa ili kukabiliana na mizozo hiyo nchi za Afrika zinahitaji kuweka sera na mikakati ya kuondoa vikwazo vya ufanyaji biashara na upitishaji wa bidhaa kwa kufungua mipaka yake.
Aidha, walishauri kuwa umefika wakati wa nchi za Afrika kuzalisha mafuta yake na kutumia vyanzo vingine mbadala vya nishati ili kukabiliana na uhaba wa mafuta na kupanda kwa bidhaa hiyo muhimu katika uzalishaji na uchumi wa mataifa hayo.

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akichangia mjadala kufuatia taarifa ya Kamisheni ya Umoja wa Mataifa inayosimamia Uchumi Afrika (UNECA), iliyochambua athari za mgogoro unaoendelea Mashariki ya Kati namna ulivyoleta athari hasi za kiuchumi na kijamii katika Bara la Afrika na namna ya kukabiliana nazo, katika Mkutano wa 58 wa Mawaziri wa Fedha, Mipango na Maendeleo ya Uchumi na Magavana wa Benki Kuu wa Afrika, unaofanyika jijini Tangier nchini Morocco.


Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akishiriki Mkutano wa 58 wa Mawaziri wa Fedha, Mipango na Maendeleo ya Uchumi na Magavana wa Benki Kuu wa Afrika wa Kamisheni ya Umoja wa Mataifa inayosimamia Uchumi Afrika (UNECA), unaofanyika jijini Tangier nchini Morocco, ambao pamoja na mambo mengine unajadili athari za mgogoro unaoendelea Mashariki ya Kati namna ulivyoleta athari hasi za kiuchumi na kijamii katika Bara la Afrika na namna ya kukabiliana nazo. Mkutano huo umewashirikisha pia Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Mipango na Uwekezaji Mhe. Dkt. Pius Chaya na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba.



















.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)

.png)







