-Agusia korosho za Tanzania zinavyopendwa nchini Urusi ,raia wa nchi hiyo walivyoonesha upendo wao kwa Rais 

-Mchambuzi wa siasa za kimataifa naye aweka wazi muonekano wa Tanzania kupitia ziara ya kihistoria

Na Said Mwishehe,Michuzi TV.

KAMA kuna jambo limeleta faraja na kuleta matumaini katika mioyo ya Watanzania basi ni hii ziara ya kihistoria iliyofanywa na Rais Dk.Samia Suluhu Hassan .

Ni ziara ambayo kwa hakika imeenda kufungua milango na fursa kwa Taifa la Tanzania na Rais Dk.Samia akiwa nchini Urusi ametoa hotuba iliyobeba maono na dhamira yake njema kwa Taifa lake na kwa kubwa zaidi kwa kuangalia maslahi mapana kwa nchi zote mbili ,Tanzania na Urusi.

Binafsi kama ilivyo kwa Watanzania wengine wengi,nimekuwa nikifuatilia kwa karibu ziara ya Rais Samia nchini Urusi pamoja na kusikiliza kwa makini yaliyozungumzwa katika ziara hiyo .Kwa mujibu wa ratiba Rais Samia anarejea nchini leo.

Hata hivyo Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Deodatus Balile ambaye ni miongoni mwa waandishi wa habari walioambatana na Rais Samia katika ziara hiyo ametumia nafasi yake kueleza kwa kina faida ya ziara ya Rais na hakika amezungumza hatua kwa hatua kuhusu aliyoyaona katika ziara hiyo.

Balile amesema ziara ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan nchini Urusi imefungua milango mipya ya biashara, uwekezaji na ushirikiano wa kiuchumi kati ya Tanzania na taifa hilo lenye ushawishi mkubwa duniani.

Anasema tayari bidhaa za Tanzania, hususan korosho, zimeanza kupata soko kubwa nchini Urusi huku wafanyabiashara wa nchi hiyo wakionyesha nia ya kuwekeza katika viwanda vya kuongeza thamani mazao hayo.

“Nipo hapa katika maduka makubwa ya biashara na nimejionea korosho kutoka Tanzania zikipewa kipaumbele.Wafanyabiashara wengi wameonyesha nia ya kuja kuwekeza katika viwanda vya kubangua na kufungasha korosho ili ziweze kuuzwa kwa ubora zaidi katika soko la Urusi,” anasema Balile.

Anaongeza mbali na korosho, wawekezaji wa Urusi wameonyesha hamu ya kuwekeza katika sekta za chai, kahawa na kilimo kwa ujumla, jambo ambalo linaweza kuwanufaisha wakulima wa kawaida na kuongeza uhakika wa masoko ya mazao ya Tanzania.

Kwa mujibu wa Balile, ziara hiyo ni ya kihistoria kwani imefanyika takribani miaka 57 baada ya ziara ya mwisho ya kiongozi wa Tanzania nchini ambayo iliyofanywa na Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere.

Balile anasema mapokezi ya Rais Samia na ujumbe wake nchini Urusi yanaonyesha namna ambavyo wananchi wa Urusi wanavyothamini uhusiano wao na Tanzania.

“Wananchi wa kawaida wameguswa sana na ujio wa Rais Samia. Wengi wanatueleza kuwa ujio huu umeonyesha kuwa bado wana marafiki wa kweli duniani. Vyombo vya habari vya Urusi vimeipa Tanzania nafasi kubwa na watu wengi wanahoji kuhusu uhusiano wetu na Urusi,” anasema Balile ambaye alieleza hayo alipokuwa akihojiwa na kituo cha redio cha U FM cha Azam Media.

Balile pia anaeleza kwamba mpango wa kuanzishwa kwa safari za ndege za moja kwa moja kati ya Tanzania na Urusi unaweza kuongeza idadi ya watalii na kuchochea biashara kati ya mataifa hayo mawili.

Akitoa tathmini yake kuhusu ziara hiyo, mchambuzi wa siasa za kimataifa na diplomasia, Godfrey Mchungu, anasema l ziara ya Rais Dk.Samia ni ya kimkakati na inaendana na mwelekeo wa Tanzania wa kuimarisha diplomasia ya uchumi.

Anasema Urusi ni moja ya mataifa yenye ushawishi mkubwa duniani katika sekta za nishati, teknolojia, biashara na siasa za kimataifa, hivyo ushirikiano wake na Tanzania unaweza kuleta manufaa makubwa ya kiuchumi.

“Hii ni ziara inayojenga msingi wa kuimarisha sera ya nje ya Tanzania kwa kuzingatia diplomasia ya uchumi. Tanzania inahitaji kushirikiana na mataifa yenye nguvu za kiuchumi na kiteknolojia ili kuongeza uwekezaji, biashara na maendeleo ya sekta mbalimbali.”

Anaongeza ushiriki wa Rais Dk.Samia katika majukwaa makubwa ya kimataifa nchini Urusi umeongeza mwonekano wa Tanzania duniani na kutoa fursa ya kutangaza vivutio vya uwekezaji vilivyopo nchini.

Kwa mujibu wa mchambuzi huyo, mafanikio ya ziara hiyo yatategemea namna ambavyo makubaliano yaliyofikiwa yatatekelezwa kwa vitendo kupitia ushirikiano wa wataalamu wa pande zote mbili.

“Ziara na mazungumzo ni hatua ya kwanza. Hatua inayofuata ni kwa wataalamu kuchakata makubaliano hayo na kuyaweka katika utekelezaji. Hapo ndipo Watanzania wataanza kuona matokeo halisi ya ushirikiano huo katika sekta za elimu, afya, teknolojia, nishati, biashara na uwekezaji,” anasema.

Ziara ya Rais Samia nchini Urusi imehusisha mikutano ya ngazi ya juu, mazungumzo ya kibiashara na uwekezaji pamoja na ushiriki katika majukwaa ya kimataifa, huku ikilenga kuimarisha uhusiano wa kihistoria kati ya Tanzania na Urusi na kufungua fursa mpya za maendeleo ya kiuchumi.

Simu 0713833822











-Uwekezaji wa Bil 49/- NIRC unavyookoa wakulima wadogo Korogwe



Na Hafidh Kido


MOSES Mdoe amesimama mbele ya mfereji unaotiririsha maji kwa kasi, sauti yake inatengeneza mwagwi unaotufanya tuzungumze kwa sauti za juu wakati wa mahojiano.

“Hii ni baraka aliyotujaalia Mungu wananchi wa Kijiji hiki. Dunia ipo kwenye mtanziko wa athari za mabadiliko ya tabianchi lakini sisi baraka ndio kama hii, maji yanatiririka tunapata mavuno,” anasema Mdoe.

Nyuma ya maneno ya faraja ya Mdoe ambaye ni Mwenyekiti wa Kijiji cha Chekelei, Kata ya Chekelei, Tarafa ya Mombo, Wilaya ya Korogwe mkoani Tanga, kuna kilio cha muda mrefu kwa wakulima wa mpunga, mbogamboga na matunda juu ya skimu kongwe ya umwagiliaji.

“Skimu ya kwanza ya jadi na miundombinu ya kienyeji ya umwagiliaji hapa Chekelei ilianza kujengwa na kutumiwa na wakulima wenyewe tangu mwishoni mwa miaka ya 1970 na mwanzoni mwa miaka 1980, ambapo wakulima walitegemea mifereji ya udongo iliyochimbwa kwa mkono kuelekeza maji kutoka milimani,” anaeleza Mdoe.

Kwa mujibu wa taarifa za Tume ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC), baada ya serikali kuona juhudi za wananchi skimu hiyo ilianza kufanyiwa maboresho rasmi ya kitaalamu kati ya mwaka 1996 na 1997, ambapo serikali kwa ushirikiano na wafadhili ikiwemo Benki ya Dunia (WB) na Mradi wa Ushirikishwaji, Maendeleo na Uwezeshaji katika Sekta ya Kilimo (PADEP) ilijenga baadhi ya mifereji ya zege ili kupunguza upotevu wa maji ardhini.

Aidha, kwa mujibu wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022, Kata ya Chekelei ina jumla ya wakazi wapatao 9,778.

Kwa miaka mingi Chekelei inafahamika ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe kama moja ya ghala la chakula au kitovu kikubwa cha uzalishaji wa nafaka, hasa mpunga.

Pamoja na mpunga, wakulima wa Chekelei wanalima mazao ya chakula kama mahindi, na mazao ya bustani ya muda mfupi kama vile matango, pilipili hoho na matikiti maji hasa kwenye maeneo yenye mwinuko kidogo kipindi cha kiangazi.

Jiografia ya Chekelei inafanya kijiji hiki kupokea maji mengi yanayotiririka kutoka safu za Milima ya Usambara.

Wakati wa mvua kubwa, maji yanakuwa mengi mabondeni, lakini changamoto kubwa ilikuwa ni kukosekana kwa miundombinu thabiti ya kuyazuia na kuyahifadhi, hivyo maji yalipita kwa wingi na kuleta athari kama mafuriko, mmomonyoko wa ardhi na kuondoa udongo wenye rutuba.

Mvua zinapokata au kuchelewa kutokana na mabadiliko ya tabianchi, wakulima hukumbana na ukame.Hali hii hulazimisha mbegu kukauka ardhini na kusababisha hasara, hivyo kuwafanya wakulima wajitegemee kwa miundombinu ya kienyeji au kubadili mazao kama kulima matikiti yanayostahimili maji kidogo.

Mwanaisha Zuberi mkazi wa Chekelei, ni mkulima wa mpunga na mahindi kwa miaka tisa sasa, anasimulia adha wanayopata kutokana na kuyumba kwa misimu ya mvua.

"Kuna miaka mvua zinakuwa nyingi sana na siku nyingine zinakuwa chache hadi hatupati chakula; kwa ufupi mvua hazina msimamo," anasema Mwanaisha.

Anaongeza kuwa kwa sasa wanategemea sana taarifa za utabiri wa hali ya hewa kutoka Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) kupitia redio, ambapo viongozi wa kijiji wanapozipata huwashauri kupanda mazao yanayohimili mabadiliko hayo.

Changamoto ya ukame wa ghafla inathibitishwa pia na Goodluck Kaoneka, mkulima wa mazao ya mboga mboga na matunda ikiwemo matango, pilipili hoho na matikiti katika kata hiyo.

Kaoneka anaeleza mvua zikikata, mbegu hushindwa kuota na kuwasababishia hasara kubwa, hatua inayowalazimu kusitisha kilimo.

"Maji yanapokata inabidi ulime katika kipindi ambacho mbegu zinaweza kutoka kwa haraka. Ndio maana tikiti halichukui maji mengi, hivyo tunalilima zaidi kipindi cha mvua chache," anabainisha Kaoneka akieleza mbinu mbadala wanazotumia sasa kujinusuru walizoelezwa na wataalamu wakilimo.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Chekelei, Mdoe anafafanua kuwa tatizo kubwa halijawahi kuwa ukosefu wa maji kabisa, bali ni ukosefu wa miundombinu ya kuyahifadhi. Wakati wa masika, maji yanakuwa mengi lakini yanapita na kuondoka kwa kasi kwa kuwa hakuna kizuizi.

"Baadhi ya miundombinu wakulima wanajitengenezea wenyewe kienyeji. Wakulima wanakuwa mabondeni na wengine wako juu, jambo linaloleta usumbufu," anasema Mdoe.


Ushirikiano kati ya wakulima na wataalamu wa kilimo umekuwa nguzo muhimu.

Mdoe anamsifia Afisa Kilimo wa eneo hilo, Juma Mashauri, akisema: "Anajitahidi sana. Hata masuala ya mbolea yanatumwa kwa njia ya ujumbe wa maandishi (SMS) kwenye simu, na anatupa muongozo kukiwa na changamoto ya wadudu au mvua kuchelewa."


NIRC inaibuka kama mkombozi

Katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi zinazotishia usalama wa chakula na ustawi wa kiuchumi nchini, Serikali ya Awamu ya Sita imeelekeza uwekezaji mkubwa wa kimkakati wa zaidi ya Shilingi bilioni 49.7 katika miradi ya miundombinu ya umwagiliaji wilayani Korogwe.

Hatua hii inalenga kuwatoa wakulima wadogo katika utegemezi wa kilimo cha mvua za msimu na kuwaingiza katika kilimo endelevu chenye tija ya kibiashara.

Kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC), miradi miwili mikuu ya Bwawa la Mkomazi na ukarabati wa skimu ya Chekelei inatajwa kuwa mkombozi wa mnyororo wa thamani wa mazao ya chakula na biashara kwa maelfu ya kaya vijiduniani.

“Mradi huu unaolenga kujibu kilio cha wakulima wa mpunga waliopo mabondeni na vilimani. Serikali imetenga kiasi kikubwa cha fedha ili kuleta suluhisho la kudumu la uhifadhi wa maji,” anasema Mkurugenzi Mkuu wa NIRC, Raymond Mdolwa.

Anafafanua kuwa mradi wa Chekelei utagharimu jumla ya Shilingi Bilioni 31.1, ambapo tayari umeshaanza kutekelezwa na umefikia asilimia 10.01.

“Mradi huu utanufaisha wananchi 4,000 katika vijiji sita vya Kata ya Chekelei. Mradi unatarajiw akuikamilika Machi 2027,” anasema Mdolwa.

Mwenyekiti Mdoe anabainisha ujenzi wa bwawa hili unaleta matumaini makubwa: "Ukikamilika huu mradi wa bwawa tutakuwa na maisha mazuri, tutalima kwa wakati na tutavuna kwa wakati."

NIRC hawajaishia hapo katika Wilaya ya Korogwe, mradi mwingine unatekelezwa Mkomazi, ambapo kwa mujibu wa NIRC mradi huu unalenga ukanda mpana zaidi wa wilaya hiyo na upo ukingoni mwa kuanza kutoa matokeo.

Gharama zake ni Shilingi Bilioni 18.6, utekelezaji wake umefikia asilimia 97 wanufaika ni wananchi 20,000 katika vijiji 28 vilivyopo katika kata saba za Wilaya ya Korogwe na unatarajiwa kukamilika Septemba mwaka huu (2026).

Kwa mujibu wa taarifa za kitaalamu kutoka NIRC, miradi hii inakwenda kuwasaidia wakulima wadogo kujipatia kipato cha uhakika zaidi kupitia kilimo cha mismu mitatu.

“Miundombinu hii itawawezesha wakulima kulima na kuvuna zaidi ya mara moja kwa mwaka, bila kusubiri wala kutegemea msimu wa mvua,” anasema Mdolwa.

Kuhama kutoka kilimo cha kienyeji cha mabondeni kwenda kwenye skimu rasmi zilizopangwa kunasaidia pia kulinda mazingira. Kunazuia uharibifu wa vyanzo vya maji na mmomonyoko wa udongo unaosababishwa na mafuriko ya msimu, huku kukihakikisha ugawaji wa maji wa usawa kati ya wakulima wa juu na wale wa chini wa skimu.

Ujenzi na ukarabati huu wa skimu za umwagiliaji wilayani Korogwe ni kielelezo tosha kuwa uhimilivu dhidi ya mabadiliko ya tabianchi unawezekana pale tu takwimu, rasilimali fedha, na ushiriki wa jamii vinapokutana pamoja.





Mwandishi wa makala haya (kulia) akiwa na mkulima wa mbogamboga na matunda, Goodluck Kaoneka. Ambaye anadai Kijiji cha Chekelei kitanufaika kiuchumi baada ya kukamilika mradi wa skimu ya umwagiliaji unaosimamiwa na Tume ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC).


Na Mwandishi Wetu.

WAKULIMA wa zao la miwa katika wilaya za Mvomero na Kilosa mkoani Morogoro wamehimizwa kutumia viuatilifu kwa usahihi na kufuata taratibu za usalama ili kujikinga na madhara yanayoweza kuathiri afya zao pamoja na mazingira.

Rai hiyo imetolewa na Mtafiti kutoka Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) Kituo cha Kibaha, Ngabo Vicent Pamba wakati wa mafunzo maalumu yaliyofanyika eneo la Mtibwa wilayani Mvomero, yakihusisha wakulima wa miwa, maafisa ugani, wauzaji wa pembejeo za kilimo pamoja na maafisa wa mazingira.

Ngabo amesema lengo la mafunzo hayo ni kuwajengea uwezo wadau mbalimbali wa mnyororo wa thamani wa zao la miwa kuhusu matumizi sahihi ya viuatilifu na namna salama ya kuhifadhi na kutupa vifungashio vya viuatilifu baada ya matumizi.

“Tuko hapa kutoa mafunzo mahususi kwa wakulima, maafisa ugani, wauzaji wa pembejeo na maafisa wa mazingira kuhusu matumizi sahihi ya viuatilifu pamoja na uhifadhi salama wa vifungashio vyake. Lengo ni kuiepusha jamii ya wakulima na madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na matumizi yasiyo sahihi ya viuatilifu,” amesema Ngabo.

Ameeleza TARI Kibaha imekuwa ikifanya tafiti mbalimbali za kuboresha kilimo cha miwa nchini na kwamba mafunzo hayo ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha wakulima wanalima kwa tija huku wakilinda afya zao na mazingira.

Aidha, amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kutoa fedha za kutosha kusaidia utekelezaji wa programu zinazolenga kuimarisha usalama wa wakulima na kuongeza tija katika sekta ya kilimo.

Kwa upande wake, Ofisa Mwandamizi kutoka Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA), Raphael Mwezi, amesema mamlaka hiyo imeungana na TARI katika kutoa elimu kwa wakulima ili kuhakikisha matumizi ya viuatilifu yanafanyika kwa kuzingatia sheria na kanuni zilizopo.

“Hili ni jukumu letu la kisheria kuhakikisha wakulima wanapata elimu ya kujikinga dhidi ya madhara ya viuatilifu. Tumekuwa tukitoa mafunzo katika vijiji mbalimbali vya wilaya ya Mvomero na sasa tunaendelea kufikia maeneo mengine ya Kilosa ili kuhakikisha wakulima wengi zaidi wananufaika,” amesema Mwezi.

Naye Ofisa Kilimo wa Mtibwa, Lucas Mtoi, amepongeza TARI Kibaha kwa kuandaa mafunzo hayo akisema yamekuwa na manufaa makubwa kwa wakulima na wataalamu wa kilimo katika eneo hilo.

“Mafunzo haya yamewasaidia wakulima kuelewa umuhimu wa kutumia vifaa kinga na kufuata maelekezo ya matumizi ya viuatilifu ili kulinda afya zao na kuongeza tija katika uzalishaji,” amesema Mtoi.

Baadhi ya wakulima walioshiriki mafunzo hayo wameeleza kufurahishwa na elimu waliyoipata na kuahidi kuitumia kuboresha shughuli zao za uzalishaji wa miwa.

Mkulima kutoka kijiji cha Luhungo, Kata ya Mtibwa, Elikunda Emmanuel Wanjama, amesema mafunzo hayo yamefungua uelewa wake kuhusu matumizi sahihi ya viuatilifu na namna ya kujikinga dhidi ya madhara yake.










NA MWANDISHI WETU – SONGEA

Serikali inaendelea kuboresha na kujenga Miundombinu ya uvuvi ikiwemo masoko ,maghala ya kuhifadhia mazao ya uvuvi, vichanja vya kukaushia samaki maghala ya kuifadhia mazao ya uvuvi na viwanda vya kuchakata mazao ya uvuvi na teknolojia rafiki za ukaushaji ili kubadilisha sekta hii kutoka ufugaji na ukulima mdogo kuelekea katika kuimarisha lishe na uchumi wa wakulima wadogo wanaojikita katika uzalishaji na ukuzaji wa viumbe maji nchini ambapo matokeo hayo yanatarajia kuchochea uchumi wa wananchi na taifa kwa ujumla.


Hayo yameelezwa na Bw. Jumanne Mwankoo Kaimu katibu Tawala Mkoa wa Ruvuma wakati wa tukio la kuhakiki taarifa ya matokeo ya mwisho ya mradi wa kuimarisha lishe kwa wakuzaji wadogo wa viumbe maji (ARNSA) uliokuwa ukiratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge Uratibu wenye Ulemavu kwa msaada wa Shirika la NORAD kupitia Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo Duniani IFAD tarehe 5 Juni 2026.Bw. Mwankoo alisema kuwa Mradi huo wa kikanda uliokuwa katika Nchi za Tanzania, Kenya na Msumbiji na kutekelezeka katika Mikoa ya Lindi Mtwara na Ruvuma nchini,



Ambao umetoa mchango mkubwa katika sekta ya uvuvi ambayo imechangia takribani asilimia 69% ya protini katika lishe bora, uzalishaji wa mazao ya viumbe maji sambamba na ongezeko la ajira kwa vijana na wanawake na kuimarisha lishe kwa wakuzaji wadogo wa viumbe maji, hususan wakulima wa mwani na wafugaji wa samaki katika Halmashauri za Mtama, Ruangwa Songea na Mbinga

Akiongea wakati wa kufunga mradi huo wa Lishe, Mratibu wa Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu Bw. Salimu Mwinjaka Alisema kuwa, mradi huo wa miaka miwili ulijikita zaidi katika katika kilimo cha mwani na uzalishaji wa viumbe maji ulifanikiwa kwa kiasi kikubwa kwani wanufaika wa mdari huo bado wanaendelea na shughuli hizo za uzalishaji kwa kutumia teknolojia za kisasa na ubunifu waliojijengea.








Kwa pande wake Mkurugenzi wa Ukuzaji viumbemaji toka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt Nazaeli Madala alieleza kuwa, Serikali imeweka msisistizo katika kukuza uchumi na mikoa iliyotekeleza mradi huo imeweza kukuza uchumi.



‘Mkoa hiyo imebahatika kupata ardhi nzuri na imekuwa fursa ya kuweza kufuga na kupata chakula na kuwauzia wengine chakula, kupata uzalishaji ulio na tija pamoja na uzalishaji Ajira na huu ndo msukomo wa Serikali.” Alibainisha Dkt Madala.
Aidha Aliwaasa wanufaika wa Mradi huo kuwapatia wengine ujuzi walioupata na kuwa waaminifu wanapopata mikopo kupitia Bank ya Kilimo nchini TADB kwa kuirejesha kwa wakati kwa amendeleo ya Taifa.Afisa Uvuvi kutoka Cameroon Bi Audrely Tchoundi aliwapongeza wafugaji wa Tanzani kwa kuwa wabunifu katika eneo la ufungaji viumbemaji na ukulima wa mwani kwa kutumia mbinu mbadala akitolea mfano wakulima wa Mwani wa Kijiji cha Shuka Mkoani Lindi, pamoja na usimamizi mzuri wa mabwawa ya samaki.

Mmoja wa wanufaika wa Mradi huo mwakilishi wa vijana Bw. Innocent Kikiwa Amesema kuwa mradi huo umemuwezesha yeye kama kijana kuweza kupata uzoefu katika eneo la Ufugaji Viumbemaji na kilimo cha mwani, kuweza kujiajiri kukuza mnyororo wa thamani kwa kuuza mazao yatokanayo na zao la mwani, kuuza samaki anaowafuga pamoja na kutafuta masoko.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Makamu wa Rais Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi pamoja na Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro mara baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere tarehe 06 Juni, 2026 baada ya kuhitimisha Ziara yake ya Kitaifa, St. Petersburg nchini Urusi tarehe 05 Juni, 2026 kufuatia mwaliko wa Rais wa Nchi hiyo Mhe. Vladmir Putin.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na viongozi mbalimbali baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere tarehe 06 Juni, 2026 baada ya kuhitimisha Ziara yake ya Kitaifa, St. Petersburg nchini Urusi tarehe 05 Juni, 2026 kufuatia mwaliko wa Rais wa Nchi hiyo Mhe. Vladmir Putin.



 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na viongozi mbalimbali baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere tarehe 06 Juni, 2026 baada ya kuhitimisha Ziara yake ya Kitaifa, St. Petersburg nchini Urusi tarehe 05 Juni, 2026 kufuatia mwaliko wa Rais wa Nchi hiyo Mhe. Vladmir Putin.

Na Pamela Mollel Arusha

Wakati Tanzania ikiendelea kujikita katika kukuza uchumi kupitia sekta ya utalii, zaidi ya washiriki kutoka nchi 50 duniani wamekutana mkoani Arusha kushiriki Maonesho ya Kimataifa ya Karibu-KiliFair yanayolenga kufungua masoko mapya na kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea nchi

Maonesho hayo yanakuja wakati serikali ikiendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuitangaza Tanzania katika masoko ya kimataifa na kuimarisha mazingira ya uwekezaji katika sekta ya utalii

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa maonesho hayo, Mkurugenzi wa Idara ya Utalii, Bi. Theresa Mugobi, aliyemwakilisha Waziri wa Maliasili na Utalii, alisema serikali imeweka mkazo katika kuboresha miundombinu ya utalii, huduma za ukarimu na viwango vya utoaji huduma ili kuifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zinazovutia zaidi watalii duniani

Alisema pamoja na kuendeleza masoko ya jadi, serikali pia inaelekeza nguvu katika kufungua masoko mapya barani Afrika, Asia, Ulaya, Mashariki ya Kati na Amerika ili kuongeza ushindani wa Tanzania katika soko la utalii duniani

Kwa mujibu wa waandaaji wa Karibu-KiliFair, maonesho hayo yameendelea kuwa daraja muhimu linalowaunganisha wanunuzi wa huduma za utalii, wawekezaji na waendeshaji wa safari kutoka mataifa mbalimbali

Mkurugenzi Mwenza wa Karibu-KiliFair, Dominic Shoo, alisema ongezeko la washiriki kutoka mataifa mbalimbali ni ishara kuwa Tanzania imeendelea kujijengea heshima kama kitovu muhimu cha biashara ya utalii katika ukanda wa Afrika Mashariki

Aliongeza kuwa ushirikiano kati ya serikali na sekta binafsi utaendelea kuwa nguzo muhimu katika juhudi za kuitangaza Tanzania na kuongeza mchango wa utalii katika uchumi wa taifa

Karibu-KiliFair imeendelea kuwa moja ya maonesho makubwa zaidi ya utalii katika Afrika Mashariki, yakitoa nafasi kwa wadau kutangaza vivutio vya utalii, kujenga mitandao ya biashara na kuibua fursa mpya za uwekezaji ndani ya sekta hiyo.









Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba ametatua mgogoro wa ardhi uliodumu kwa miaka 41 kati ya Kanisa Katoliki Parokia ya Mtakatifu Yohana Mtume Nyololo wilayani Mufindi Mkoa wa Iringa na Familia ya Yosefa Mgavilenzi ambaye ni msimamizi wa mirathi ya marehemu Michael Bakari Seveyage.

Akihutubia mkutano wa hadhara katika kata ya Igowole Mufindi Kusini, Waziri Mkuu alipokea malalamiko ya familia ya Yosefa Mgavilenzi kuwa eneo lake lenye ukubwa wa ekari 107 limechukuliwa na Kanisa hilo bila fidia na aliomba Waziri Mkuu amsidie ili alipwe.

Mapema wiki hii Waziri Mkuu alituma timu ya wataalamu kutoka ofisi yake ambao walikwenda katika kata ya Nyololo na kufanya vikao vya maridhiano na viongozi wa Kanisa Katoliki, familia ya Yosefa, Wazee, viongozi wa Kata ya Nyololo na kijiji cha Nyololo Shuleni walioko madarakani na wastaafu pamoja na wananchi.

Baada ya majadiliano yaliyochukuwa siku tatu pande mbili husika zilikubaliana kumaliza mgogoro kwa njia ya maridhiano ambapo Baba Askofu wa Jimbo la Mafinga, Vicent Mwagala alitoa shilingi milioni 20 kama fidia kwa familia ya Yosefa ambayo ilizipokea kwa moyo mkunjufu na kukubali kumaliza mgogoro huo.

Hati za maridhiano zilitiwa saini na Kanisa Katoliki Parokia ya Nyololo pamoja na familia ya marehemu Michael Bakari Seveyage leo Juni 5, 2026 katika kikao cha maridhiano kilichofanyika kwenye Ofisi ya Mtendaji wa Kata ya Nyololo wilayani Mufindi.

Paroko wa Parokia ya Yohana Mtume Nyololo alimshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hasan kwa sera yake ya maridhiano ambayo imemuwezesha Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba kuumaliza mgogoro uliodumu kwa miaka 41.

Alimshukuru Askofu wa Jimbo la Mafinga Vicent Mwagala kwa kutoa shilingi milioni 20 kama fidia kwa mlalamikaji hatua ambayo imesaidia sana kufikia maridhiano na alisisitiza kwamba mgogoro huo umeisha na sasa wataishi kwa amani kama jamii moja.

Mchungaji John Mbwiga ambaye ni Kiongozi wa familia ya mlalamikaji aliishukuru serikali kupitia kwa Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba aliyetuma timu ya watalaamu kutoka ofisini kwake ambao wamemaliza mgogoro huo ulioikosesha familia amani kwa miaka mingi na kwamba sasa wataishi kwa amani.

Mwenyekiti wa Kijiji Mstaafu wa kijiji cha Nyololo Shuleni, Jeremia Mngolage alliishukuru serikali hususan Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba kwa kazi anayofanya ya kutatua migogoro mbalimbali katika jamii kwa njia ya mardhiano.







WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka watumishi wa umma kote nchini watambue na wathamini nafasi za kazi walizonazo kwamba ni huduma wanazotakiwa kuzitoa kwa wananchi.

“Ninapokuwa kwenye hizi ziara, nimekuwa ninawaambia watumishi wenzangu walioko maofisini kwamba kuwa kwenye hizi nafasi ni huduma, ni utumishi na kuwazungusha watu wanapotaka hizo huduma ni ushamba,” alisema. 

Waziri Mkuu alitoa wito huo jana jioni (Ijumaa, Juni 05, 2026) wakati akizungumza na wakazi wa Jimbo la Isimani katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa kijiji cha Isimani, Kata ya Kihorogota, Wilaya ya Iringa, Mkoani Iringa.

“Tutahakikisha hoja zote zinazotolewa na wananchi zinafanyiwa kazi kwa sababu huo ndiyo wajibu wa Serikali kuwatimizia wananchi yale yaliyo mahitaji yao ya kila siku ili waweze kufanya kazi wakiwa na utulivu. Nitoe rai kwa ofisi zote za umma, tuyazingatie hayo,” alisisitiza.

Aliwataka watumishi wa umma waache kupuuza haki za wananchi na hasa katika maeneo ambayo mhimili wa mahakama unakuwa umetoa haki hizo. “Kuna maeneo unakuta mahakama imetoa haki lakini baadhi ya watumishi wanakuwa na kiburi na wanapuuzia. Hili halikubaliki. Hili si ombi. Wanaokaidi nimekuja na dawa yao. Lazima tukubali kuwa mtu atapata tabasamu kama haki yake anaipata.”

Alisema baada ya kukamilisha ziara zake kwenye mikoa 10, Waziri Mkuu ataitisha kikao mubashara kwa njia ya mtandao ili kupokea taarifa ya kila mkoa jinsi ulivyotatua kero za wananchi zilizoibuliwa katika mikoa yao. “Nitataka kujua yapi yaliibuliwa, yapi yamefanyiwa kazi na yapi yamekwama na kama yamekwama ni kwa nini,” alisema.

Mpaka sasa, Waziri Mkuu amekwishazuru mikoa ya Tanga, Kilimanjaro, Arusha, Manyara, Rukwa, Katavi, baadhi ya wilaya za mikoa ya Dodoma na Singida na leo atahitimisha wilaya za mkoa wa Iringa.

Mapema, Mbunge wa Isimani, Emmanuela Mtatifikolo ambaye aliapishwa jana, aliomba jimbo hilo lipatiwe hadhi ya kuwa na Halmashauri ya Wilaya kutokana na jiografia yake ili kusogeza huduma kwa wananchi.

Akitoa mfano, mbunge huyo alisema: “Baadhi ya wananchi kutoka Maperamengi wanapotaka kwenda Ihemi zilipo ofisi za Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, wanalazimika kupanda boti (kuvuka bwawa la Mtera) hadi Migori ili waweze kupata usafiri wa magari. Wanapita Iringa mjini kabla ya kufika huko na umbali wa safari hiyo unagharimu sh. 60,000/-.” 

Aliomba pia wajengewe vituo vya afya kwenye kata za Nyang’olo na Izazi ili viweze kutoa huduma kwa wananchi wa maeneo hayo lakini pia kuhudumu nyakati za dharura endapo kutatokea ajali katika mlima Nyang’olo. 




Na Karama Kenyunko Michuzi Tv
WAZIRI katika Ofisi ya Rais anayeshughulikia Maendeleo ya Vijana, Joel Nanauka, amewataka vijana nchini kuzingatia elimu ya fedha akisema ni nyenzo muhimu ya kuwawezesha kiuchumi na kuwapa uwezo wa kushiriki kikamilifu katika agenda ya maendeleo ya taifa.

Nanauka ametoa wito huo leo Mei 5, 2026 wakati akizindua tawi jipya la Benki ya Ushirika (Coop Bank) jijini Dar es Salaam, ambalo ni tawi la sita la benki hiyo tangu kuanzishwa kwake.

Uzinduzi huo umeambatana na kusainiwa kwa makubaliano ya ushirikiano kati ya Coop Bank na Wizara ya Maendeleo ya Vijana yenye lengo la kuwajengea vijana maarifa ya kifedha na kuongeza ushiriki wao katika miradi mbalimbali ya maendeleo.

Akizungumza katika hafla hiyo, Nanauka amesema Coop Bank ni daraja muhimu linalowaunganisha vijana na fursa za kiuchumi pamoja na miradi ya maendeleo.
"Elimu ya fedha ni muhimu kwa vijana ikiwa wanataka kuwa huru kiuchumi na kuchangia kwa maana katika maendeleo ya taifa," amesema.

Ameongeza kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira rafiki yatakayowawezesha vijana kushiriki kikamilifu katika ukuaji wa uchumi wa nchi.
Aidha, aliwahimiza vijana kujiunga na mifumo rasmi ya kiuchumi na taasisi mbalimbali, akieleza kuwa hatua hiyo itawasaidia kukidhi vigezo vya kupata huduma za kifedha ikiwemo mikopo.

Mtendaji Mkuu wa Coop Bank, Godfrey Ng’urah, amesema tawi la Dar es Salaam ni la nne kufunguliwa mwaka huu. Alibainisha kuwa benki hiyo ilianza shughuli zake ikiwa na matawi matatu katika mikoa ya Mtwara, Kilimanjaro na Dodoma.

Ng’urah amesema benki hiyo inapanga kufungua jumla ya matawi 12 kabla ya mwisho wa mwaka kama sehemu ya mkakati wake wa kusogeza huduma katika vituo vikuu vya biashara nchini.

"Dhamira yetu ni kutoa suluhisho za kifedha kwa Watanzania kwa wakati na kwa kusogeza huduma za benki karibu zaidi na wananchi," amesema.

Ameongeza kuwa kupitia mfumo wa ushirika, benki hiyo inaamini kuwa ifikapo mwaka 2030 itakuwa imeongeza kwa kiasi kikubwa idadi ya wateja wake huku ikitumia teknolojia kuhamasisha maendeleo ya vijana na ujumuishaji wa kifedha.

Pia amesema Coop Bank iko tayari kushirikiana na taasisi za serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo katika juhudi za kuharakisha maendeleo ya taifa.
Naye, Mwenyekiti wa Bodi ya Coop Bank, Dkt.Joseph Witts, amesema benki hiyo imejizatiti kuunda fursa zitakazowasaidia vijana kuboresha hali zao za kiuchumi.
"Dar es Salaam inachangia kwa kiasi kikubwa uchumi wa taifa na ina fursa nyingi za uwekezaji na biashara," alisema.

"Kufunguliwa kwa tawi katika jiji hili kutafanya huduma za kifedha zipatikane kwa urahisi zaidi kwa wawekezaji, wafanyabiashara na wateja wetu wanaoongezeka."

Dkt. Witts alisema lengo kuu la benki hiyo ni kuweka maslahi ya wanachama wake mbele huku ikihakikqisha ukuaji endelevu na upanuzi wa shughuli zake.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Tume ya Maendeleo ya Ushirika, Abulmajid Nsekela, ambaye pia ni Mtendaji Mkuu wa CRDB Bank, amesema kuendelea kwa upanuzi wa Coop Bank ni mafanikio makubwa kwa harakati za ushirika nchini Tanzania.

"Ufunguzi wa tawi hili la Dar es Salaam ni hatua chanya na ni fursa ya kuhudumia vyama vingi vya ushirika vinavyofanya kazi katika jiji hili," alisema.

Pia amesisitiza umuhimu wa utawala bora, usimamizi madhubuti na matumizi ya teknolojia katika utoaji wa huduma bora za kifedha kwa Watanzania.
Kwa sasa, Coop Bank inaendesha matawi sita yaliyopo Dar es Salaam, Dodoma, Moshi, Tabora na matawi mawili mkoani Mtwara.





Wadau wa sekta ya ushirika mkoani Dodoma wamekutana katika Jukwaa la Maendeleo ya Ushirika Mkoa wa Dodoma kujadili utekelezaji wa maazimio yaliyopitishwa katika mikutano iliyopita, huku wakitathmini mafanikio yaliyopatikana na kuweka mikakati mipya ya kuimarisha vyama vya ushirika katika mkoa huo.

Akizungumza Juni 5, 2026, katika jukwaa hilo, Mrajisi Msaidizi wa Vyama vya Ushirika Mkoa wa Dodoma, Joseph Chintika, amesema jukwaa hilo ni la tano tangu kuanzishwa kwa utaratibu wa kuwakutanisha wadau wa ushirika kwa lengo la kujadili maendeleo, changamoto na fursa zilizopo katika sekta hiyo.

Amesema ushirika wenye mafanikio unategemea ushiriki wa wanachama wake na kuwataka washiriki kutumia nafasi hiyo kujadili kwa uwazi masuala yanayoikabili sekta hiyo ili kupata suluhisho la pamoja.

Chintika amesema serikali itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha vyama vya ushirika vinakuwa imara, vinazingatia sheria na kanuni zilizowekwa na vinatoa manufaa kwa wanachama wake pamoja na jamii kwa ujumla.

Katika mjadala uliofanyika, wadau mbalimbali wameeleza kuwa bado kuna changamoto zinazovikabili vyama vya ushirika, wamesema utekelezaji wa maazimio ya jukwaa hilo utasaidia kuimarisha utendaji wa vyama hivyo na kuongeza mchango wake katika maendeleo ya uchumi wa wananchi na Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake, mwakilishi kutoka Chuo Kikuu cha Ushirika Moshi (MOCU), Fredy Lyimo, amesema kujenga uaminifu miongoni mwa wanachama, viongozi na watendaji ni hatua muhimu katika kuhakikisha vyama vya ushirika vinaendelea kuwa imara na endelevu, ameongeza kuwa utekelezaji sahihi wa sera, sheria, kanuni na miongozo ya ushirika ni msingi wa mafanikio ya taasisi hizo.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Climb Up Limited, Emmanuel Ngallah, ameeleza umuhimu wa matumizi ya teknolojia, na mizani janja ya kidigitali, katika shughuli za ushirika,itaweza kusaidia kuongeza uwazi, kurahisisha utunzaji wa kumbukumbu na kuboresha utoaji wa huduma kwa wanachama.

Mkoa wa Dodoma una zaidi ya vyama vya ushirika 130 vinavyohudumia sekta mbalimbali za uzalishaji na biashara, wadau wa jukwaa hilo wameeleza matumaini yao kuwa kupitia majadiliano na utekelezaji wa maazimio yaliyofikiwa, vyama hivyo vitaendelea kuwa nguzo muhimu ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa mkoa huo.

Kaulimbiu ya Maendeleo ya Ushirika kwa mwaka 2026 inasema, “Ushirika kwa Dunia Yenye Amani; Linda Ushirika, Chagua Uadilifu,” ikisisitiza umuhimu wa maadili na uwajibikaji katika kuimarisha harakati za ushirika nchini.


Taasisi ya INADES Formation Tanzania imeadhimisha Siku ya Mazingira Duniani kwa kupanda miti 200 ya kivuli na matunda katika Shule ya Sekondari Kisima cha Ndege iliyopo Wilaya ya Bahi mkoani Dodoma.

Zoezi hilo ni sehemu ya mwendelezo wa kampeni ya “Panda Mti Tuilinde Kesho” iliyozinduliwa Januari 2026, yenye lengo la kuchangia juhudi za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na kuimarisha utunzaji wa mazingira.

Akizungumza baada ya shughuli ya upandaji miti iliyofanyika Juni 5, 2026, Mwakilishi wa INADES Formation Tanzania, Paul Ephras Chugu, amesema taasisi hiyo imefanikiwa kupanda miti zaidi ya 15,000 katika vijiji vinne vya Wilaya ya Bahi tangu kuanza kwa kampeni hiyo.

Kwa upande wake, Afisa Mazingira wa Halmashauri ya Wilaya ya Bahi, Joyce Anania Jackson, ameipongeza INADES Formation Tanzania kwa ushirikiano mzuri unaoendelea kati ya taasisi hiyo na halmashauri katika kutekeleza shughuli za uhifadhi wa mazingira.

Naye Mkuu wa Shule ya Sekondari Kisima cha Ndege,  Mwalimu wa Mazingira na Mwenyekiti wa Klabu ya Mazingira wa shule hiyo, wamepongeza juhudi za taasisi hiyo kwa kuendelea kutoa elimu na kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa utunzaji wa mazingira.

Maadhimisho hayo ya Siku ya Mazingira Duniani yaliambatana na bonanza la michezo lililowakutanisha wanafunzi wa shule hiyo, wanafunzi kutoka shule jirani pamoja na wananchi wa vijiji vya jirani, kwa lengo la kutoa elimu kuhusu uhifadhi wa mazingira na kuhamasisha ushiriki wa jamii katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.






Top News