Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga (Mb), amewataka Watanzania kuendelea kutembelea Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), akisema maonesho ya mwaka huu 2026 yameonesha mafanikio makubwa ya maendeleo ya viwanda, ubunifu wa teknolojia na ubora wa bidhaa zinazozalishwa nchini.

Akizungumza Julai 08, 2026 baada ya kutembelea mabanda mbalimbali ya maonesho hayo, Kapinga amesema mwitikio wa wananchi ni mkubwa kiasi kwamba Serikali inatafakari kuongeza siku moja ya maonesho ili kutoa nafasi kwa wananchi wengi zaidi kushiriki na wafanyabiashara kuendelea kufanya biashara.

Amesema ukubwa wa maonesho hayo unamlazimu kuyatembelea mara kwa mara kwa kuwa haiwezekani kuona mabanda yote kwa siku moja, huku akieleza kuridhishwa na namna waoneshaji walivyojiandaa na ubora wa bidhaa zinazooneshwa.

Waziri Kapinga amesema maonesho ya mwaka 2026 yamebeba teknolojia mbalimbali za kisasa, ikiwemo magari yanayotumia umeme, magari ya mseto (hybrid), magari yanayotumia gesi asilia (CNG) kwa asilimia 100 pamoja na mitambo ya kisasa inayotumia umeme, hatua inayoonesha ukuaji wa sekta ya viwanda na matumizi ya teknolojia rafiki kwa mazingira.

Aidha, amesema bidhaa za ndani zimeendelea kuongezeka ubora, hususan katika thamani na vifungashio, jambo linalodhihirisha mafanikio ya uwekezaji wa Serikali katika kuwawezesha wananchi kiuchumi na kukuza uzalishaji wa ndani.

"Wananchi waendelee kujitokeza kutembelea Sabasaba. Fursa zilizopo mwaka huu ni nyingi zaidi, hivyo ni wakati mzuri wa kujifunza, kufanya biashara na kuona maendeleo ya viwanda vya Tanzania," amesema Kapinga.

Ameongeza kuwa iwapo uamuzi wa kuongeza siku moja ya maonesho utapitishwa, utalenga kuwapa wananchi, hasa wanaokuwa kazini siku za kawaida, nafasi zaidi ya kutembelea maonesho hayo na kunufaika na fursa mbalimbali za biashara na uwekezaji.

Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Juma Zuberi Homera, amewataka watumishi wa sekta ya afya nchini kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi, uadilifu na kuzingatia maadili ya utumishi wa umma ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za afya.

Akizungumza Leo Julai 8,2026 wakati wa uzinduzi wa Kituo cha Afya Kasu kilichopo Kijiji cha Kasu, Kata ya Kandasi, Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi mkoani Rukwa, Dkt. Homera amesema Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaendelea kuwekeza katika kuboresha huduma za afya kwa kujenga na kuboresha miundombinu ya kutolea huduma karibu na wananchi.

Amesema ujenzi wa kituo hicho umegharimu takribani shilingi bilioni 1.8, huku Serikali pia ikipanga kujenga barabara ya kiwango cha lami yenye urefu wa kilomita moja kuelekea kituoni hapo kwa gharama ya takribani shilingi milioni 500, hatua itakayorahisisha upatikanaji wa huduma za afya.

Wananchi wa eneo hilo wameishukuru Serikali kwa kukamilisha mradi huo, wakieleza kuwa utapunguza umbali waliokuwa wakitembea kufuata huduma za afya na kuboresha huduma za mama na mtoto pamoja na huduma nyingine muhimu.




Jane Mwakyoma-Rukwa.

SERIKALI  imetoa siku kumi na nne (14) kwa halmashauri ya wilaya ya Nkasi mkoani Rukwa kuanza kutoa  huduma za matibabu kwa wananchi katika kituo cha Afya Chala .

Akitoa maagizo hayo Waziri wa katiba na sheria Juma Homera baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa kituo cha Afya Chala amesema  baadhi ya mjengo yamekamilika hakuna budi kuanza kufanya kazi na wananchi waendelee kupata huduma katika kituo hicho.

Amesema serikali ya awamu ya sita imejizatiti kuhakikisha huduma za Afya zinatolewa karibu ili kuondoa kero na adha ya kufuata huduma hiyo mbali na makazi ya wananchi.

Aidha Homera ameonya watumishi wa Afya wanaojichukulia fedha kwa wananchi kinyume na taratibu kuacha kuwatoza fedha na badala yake wafanye kazi kwa weledi na kinidhamu na kufuata taratibu zilizowekwa.

Akiwasilisha gharama za ujenzi kwa Waziri wa katiba na sheria Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Nkasi Emmanuel Masaga amesema walipokea fedha sh. 250,000,000 kwaajili ya ujenzi wa jengo la kuhudumia wagonjwa wa nje (OPD), choo cha nje na kichomea taka .

Aidha amesema mradi huo unatekelezwa kwa kutumia mfumo wa FORCE ACCOUNT ambapo mradi huo upo hatua ya umaliziaji na fedha iliyotumika ni shilingi 248,391,255.13 ikiwa fedha iliyobaki shilingi 1,608,744.87 kwaajili ya malipo ya fundi ujenzi.

Pia Masaga amemshukuru Dk.Samia Suluhu Hassan kwa kuwaletea vifaa tiba vyenye thamani ya shilingi 290,669,216.98 katika kituo hicho.

Kwaupande wake diwani wa kata ya Chala Bosco Wazamani amemshukuru Dk. Samia Suluhu Hassan kwa juhudi anazofanya kuhakikisha wananchi wake wanapata huduma bora na za uhakika.

Amesema kujengwa kwa kituo cha Afya katika kata hiyo ni ukombozi tosha kwa wananchi na itakwenda kutatua changamoto ya kutembea umbali mrefu kufuata huduma hiyo.






Kaimu Mkurugenzi mkuu wa Mamlaka ya Ukaguzi wa Vyama vya Ushirika COASCO, CPA Jeremiah Mugeta, amesema Kilimo kinamchango mkubwa katika uchumi wa nchi, kwa mujibu wa Takwimu zilizopo zinaonyesha kwamba kilimo pekee kinachangia zaidi ya asilimia 26 katika pato la Taifa, jambo ambalo ni kubwa na lakujivunia na kuona namna ambavyo ushirika unachangia kwenye maendeleo ya uchumi.

Akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), Julai 8, 2026, Mugeta amesema mchango wa sekta ya ushirika katika maendeleo ya uchumi ni mkubwa, ambapo mazao yanayouzwa kupitia vyama vya ushirika huchangia zaidi ya dola za Marekani bilioni 2 kwa mwaka, jambo linaloonesha umuhimu wa ushirika katika kukuza uchumi wa nchi.

Akizungumzia suala la ukaguzi wa vyama vya ushirika amesema wamejipanga kuhakikisha ushirika unazidi kuwa imara, na wauhakika huku malengo Yao na mipango Yao ni kuhakikisha wanaushirika wanapata elimu bora pamoja na misingi na kanuni na taratibu za kuendesha vyama vya ushirika,

Aidha CASCO kila mwaka huwa wanaandaa taarifa ya jumla ya kuonyesha matokeo ya jinsi ambavyo vyama vya ushirika vilivyofanya shughuli zake kila mwaka, na kutoa maoni katika ukaguzi wanaoufanya.

Vilevile amebainisha mpango walionao katika mwaka wa fedha 2026/2027, wamejipanga kuhakikisha vyama vyote vya ushirika vinakaguliwa ili kuweza kuwapa fursa wanaushirika kujua maendeleo ya shughuli wanazofanya kwenye vyama hivyo,

Ameeleza mkakati uliopo ni kushirikiana na Tume ya maendeleo ya ushirika, kuhakikisha vyama na viongozi wa vyama vya ushirika wanapata taarifa Sahihi ya watu gani watakaguliwa na ukaguzi huo unatarajiwa kuanza mwezi huu wa Julai kuanzia tarehe 20.

Ametoa wito kwa wanaushirika ni kuhakikisha wanaandaa taarifa za fedha za mwaka 2025/2026 na kuziwasilisha katika ofisi za COASCO zilizopo kwenye mikoa Yao ili ukaguzi uwafikie kwa wakati, na wahakikishe wanazingatia sheria na kanuni za kuandaa taarifa za fedha ili kupunguza hati chafu katika ukaguzi.







Na Mwandishi Wetu.

Zanzibar. Equity Group, kwa kushirikiana na Mamlaka ya Kukuza Uwekezaji Zanzibar (ZIPA), imeongoza ujumbe wa viongozi na wadau kutoka Tanzania Bara na Zanzibar kutembelea mradi wa Bandari ya Fumba, hatua inayolenga kuhamasisha uwekezaji na kuonyesha fursa za maendeleo ya kiuchumi zilizopo visiwani humo.

Ziara hiyo ni sehemu ya juhudi za kuwaleta pamoja wawekezaji na taasisi za Serikali ili kuimarisha mazingira ya biashara na kuongeza uwekezaji katika miradi ya kimkakati itakayochochea ukuaji wa uchumi.

Equity Bank, ambayo ni mmoja wa wafadhili wakuu wa mradi wa Bandari ya Fumba, imesema itaendelea kuunga mkono uwekezaji katika miundombinu yenye uwezo wa kuchochea biashara, kuongeza ajira na kuimarisha ushindani wa Zanzibar na Tanzania katika soko la kikanda na kimataifa.

Benki hiyo imeeleza kuwa dhamira yake inaenda zaidi ya utoaji wa huduma za kifedha, kwa kuwezesha ushirikiano kati ya wawekezaji wa ndani na wa kimataifa pamoja na mamlaka za udhibiti ili kujenga mazingira rafiki ya uwekezaji.

Aidha, juhudi hizo zinaunga mkono utekelezaji wa Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA), kwa lengo la kuimarisha biashara ya kikanda, kuvutia mitaji mipya na kufungua fursa zaidi za maendeleo ya uchumi endelevu nchini Tanzania na barani Afrika.


OFISA Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) CPA. Nicodemus Mkama amesema mafanikio ya asilimia 760.78, yameifanya Hatifungani ya iTrust kuweka historia ya kuwa Hatifungani iliyopata mafanikio makubwa zaidi kupita hatifungani zote zilizowahi kutolewa hapa nchini. 

Amesema hatifungani iliyokuwa inashikilia rekodi hiyo, ni Hatifungani ya kampuni ya First Housing Finance Limited yaani MAKAZI Bond ambayo ilipata mafanikio ya asilimia 661.1 na kuorodheshwa kwenye Soko la Hisa tarehe 09 Juni 2026 huku akiipongeza iTrust kwa kuvunja rekodi na kuendelea kuweka rekodi za mafanikio katika masoko ya mitaji.

CPA.Mkama ameyasema hayo leo Julai 8,2026 jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya kuorodheshwa kwa Hatifungani ya Kampuni ya iTRUST Finance Limited katika Soka la Hisa Dar es Salaam 

“Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) pamoja na wadau wote wa sekta ya masoko ya mitaji tumefurahishwa sana na hatua hii, na tunatoa pongezi za dhati kwa Bodi na Menejimenti ya iTrust Finance Limited, wataalamu wote waliohusika kwa kuweka rekodi hii ya kihistoria.”

Amesema iTrust Finance Limited imeendelea kuwa mfano bora na wa kuigwa kwa kampuni na taasisi katika sekta ya umma na binafsi, kwani kampuni hiyo imekuwa ikitumia vizuri fursa zinazopatikana katika masoko ya mitaji kupata rasilimali fedha za kukuza na kuendeleza biashara; kuimarisha utendaji wa Kampuni; na kugharamia shughuli za maendeleo.

“Tangu mwaka 2021 (wakati huo kampuni hii ikitumia jina la Imaan Finance Limited) na hadi hivi sasa ikiwa na jina la iTrust Finance Limited, Kampuni hii imetumia fursa za masoko ya mitaji kwa njia ya utoaji wa Hatifungani, Sukuk na Mifuko ya Uwekezaji wa Pamoja.

Akifafanua zaidi amesema hatifungani hiyo ni ya kipekee na muhimu katika maendeleo na ustawi wa masoko ya mitaji, sio tu Tanzania, bali katika ukanda wa Afrika Mashariki, kwani hatifungani hii inaweka historia na rekodi kuu Tatu,

Amesema ni hatifungani ya kwanza (1) kuorodheshwa kwenye Soko la Hisa la Dar es Salaam, ikiwa imetolewa na kampuni yenye Leseni ya Uwakala wa Soko la Hisa (Licensed Broker/Dealer); na Leseni ya Usimamizi wa Mifuko ya Uwekezaji (Fund Manager) iliyotolewa na CMSA.

Pia ni hatifungani ambayo mauzo ya toleo la kwanza yameweza kuzidi kiasi cha Programu nzima ya Hatifungani yenye Thamani ya shilingi bilioni 100 zilizokuwa zitolewe katika awamu nne ndani ya miaka minne (bilioni 15, 20, 30 na 35, katika mwaka 2026, 2027, 2028 na 2029 mtawalia).

“Kama tulivyoshuhudia mauzo ya Hatifungani ya iTrust yamepata mafanikio ya asilimia 760.78, ambapo kiasi cha shilingi bilioni 114.12 kimepatikana, ikilinganishwa na shilingi bilioni 15 zilizotarajiwa,”amesema.

Akieleza zaidi amesema mojawapo ya malengo ya DIRA ya Taifa ya Maendeleo (DIRA 2050) ni kuona kuwa Sekta ya Fedha, inawezesha upatikanaji wa rasilimali fedha kwa ajili ya kukuza na kuendeleza biashara ambazo zinachangia ukuaji na ustawi wa sekta binafsi;

sekta ya umma na uchumi wa nchi kwa ujumla hapa nchini. 

“Hivyo basi, juhudi za iTrust Finance Limited zinatoa mchango katika utekelezaji wa malengo haya, na ni hatua madhubuti ya kuongeza fursa za uwekezaji katika masoko ya mitaji na kuleta matokeo chanya kwenye uchumi wa nchi yetu.”

Pia amesema kati ya wawekezaji waliowekeza kwenye hatifungani ya iTrust, asilimia 66.66 ni wawekezaji mmoja mmoja yaani Retail Investors na asilimia 33.34 ni Kampuni na Taasisi yaani Institutional investors . 

Aidha, asilimia 98.82 ni wawekezaji wa ndani na asilimia 1.18 ni wawekezaji wa kigeni huku akifafanua kuorodheshwa kwa hatifungani hiyo kunaongeza thamani ya uwekezaji katika Hatifungani za Kampuni na Taasisi kwa asilimia 5.46 na kufikia shilingi trilioni 2.20, kutoka shilingi trilioni 2.09. 

“Ushiriki mkubwa wa wawekezaji mmoja mmoja wa ndani ni hatua muhimu katika kuongeza ukwasi (liquidity) katika soko la hisa. Aidha, hii sehemu muhimu ya utekelezaji wa Mpango Jumuishi wa Huduma za Kifedha yaani National

Financial Inclusion Framework wenye lengo la kuongeza ushiriki wa wananchi kwenye sekta rasmi ya fedha.

“Takribani asilimia 89 ya maombi yote ya uwekezaji kwenye Hatifungani ya iTrust

yamefanyika na kupokelewa kupitia mifumo ya kidijitali, ambapo mfumo wa kidijitali wa iTrust App pekee umechangia zaidi ya asilimia 71 ya maombi yote.”

CPA.Mkama amesema mafanikio hayo ni uthibitisho wa imani ya waliyonayo wawekezaji kwa Kampuni ya iTrust Finance Limited na masoko ya mitaji nchini. Aidha, mafanikio hayo ni matokeo ya mazingira wezeshi ya kisera, kisheria na kiutendaji yanayotolewa na Serikali katika masoko ya mitaji. 




▪️Yaonesha nia ya kushirikiana na Serikali katika usafiri ya Mijini.

▪️Dkt. Mwigulu awahakikishia mazingira bora ya uwekezaji

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amekutana na Makamu wa Rais wa Kampuni ya ALSTOM ya nchini Ufaransa, Philippe Deller ambapo wamejadiliana kuhusu fursa za uwekezaji katika sekta ya miundombinu ya usafiri nchini Tanzania.

Katika mazungumzo hayo, Dkt. Mwigulu Nchemba aliikaribisha ALSTOM kuwekeza nchini, akieleza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wawekezaji na kutekeleza mageuzi yanayolenga kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha biashara, usafiri na uwekezaji katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Kwa Upande wake Bw. Phillepe alieleza nia ya kampuni hiyo kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya usafiri wa mijini.

Kampuni hiyo imeonesha utayari wa kuwekeza katika ujenzi wa mifumo ya usafiri wa haraka na miundombinu ya kisasa yenye lengo la kupunguza msongamano wa magari katika Jiji la Dar es Salaam, huku ikitazama pia fursa za utekelezaji wa miradi kama hiyo katika majiji ya Mwanza, Mbeya na Arusha.

Miradi hiyo inatarajiwa kuongeza ufanisi wa usafiri wa mijini, kupunguza muda wa safari, kuimarisha shughuli za biashara na uwekezaji, pamoja na kuchochea ukuaji wa uchumi na kuboresha maisha ya wananchi kupitia matumizi ya teknolojia za kisasa.

Mazungumzo hayo ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuimarisha ushirikiano na kampuni kubwa za kimataifa ili kuleta teknolojia, utaalamu na mitaji inayochochea maendeleo ya miundombinu na uchumi wa Taifa.

Kampuni ya ALSTOM, ina uzoefu mkubwa katika kubuni, kujenga na kuendesha mifumo ya kisasa ya usafiri wa umma ikiwemo reli za kisasa, treni za mwendo kasi, metro, tram na teknolojia za usimamizi wa usafiri.






-Ni kuanzia Agosti 12,Rais Samia na Rais Mwinyi kuongoza washiriki wakati wa tamasha

-Miradi ya maendeleo kuzinduliwa,fursa mbalimbali kuibuliwa


Na Said Mwishehe,Michuzi TV-Zanzibar

KIZIMKAZI Kumenoga! Hiyo ndio kauli mbiu iliyobeba Tamasha la Kizimkazi 20226 linatarajiwa kufanyika kuanzia Agosti 12 hadi Agosti 14 mwaka huu likiwa limesheheni fursa lukuki .

Katika tamasha hilo ambalo limejizoelea umaarufu mkubwa pia kutakuwa maonyesho, burudani na programu mbalimbali za kuvutia zinazolenga kutangaza utalii, uwekezaji na utamaduni wa Kizimkazi.

Akizungumza kuhusu maandalizi ya kuelekea tamasha hilo Wilaya ya Kusini Unguja visiwani Zanzibar leo Julai 8,2026 Mwenyekiti wa Kamati ya Tamasha la Kizimkazi Mahfodh Said Omar amesema katika tamasha hilo miradi mbalimbali ya maendeleo itazinduliwa.

Katika uzinduzi wa tamasha la Kizimkazi litafunguliwa rasmi na Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Dk.Ali Hussein Mwinyi na kisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Samia Suluhu Hassan atakuwa mgeni katika siku ya kufunga tamasha hilo.

“Tunawaalika wawekezaji, wadau wa mandeleo, wafanyabiashara, wadau wa utalii na wananchi kwa ujumla kushiriki Kizimkazi Festival 2026, kwani mwaka huu tamasha limenoga na limebeba fursa nyingi kwa wote.

“Leo tunazindua rasmi maandalizi ya Kizimkazi Festival 2026. Tamasha hili lilianzishwa na wazee pamoja na wananchi wa Kizimkazi kwa lengo la kuhifadhi na kuenzi utamaduni, mila na desturi za eneo letu. Kadiri miaka ilivyopita, tamasha limeendelea kukua na sasa limekuwa jukwaa muhimu la kutangaza utalii,uwekezaji na mendeleo ya jamii.

“Kizimkazi Festival ni tamasha la wananchi wa Kizimkazi. Dhamira yake ni kuitangaza Kizimkazi kama eneo lenye historia, utamaduni, vivutio vya utalii na fursa nyingi za uwekezaji kwa manufaa ya Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ujumla.”

Kuhusu malengo ya Tamasha la Kizimkazi amesema ni kutangaza fursa za uwekezaji, kutangaza vivutio vya utalii pamoja na kuhifadhi na kuenzi utamaduni wa Kizimkazi.

Wakati kwa upande wa fursa za uwekezaji ni Utalii na hoteli, Uchumi wa Buluu, Uvuvi, Biashara na huduma mbalimbali, pamoja na miradi mingine ya mandeleo.

Akizungumzia miradi itakayozinduliwa wakati wa tamasha la Kizimkazi ni uzinduzi wa mradi wa maji Kizimkazi, uzinduzi wa kiwanja cha watoto Kibu Teni,ufunguzi wa nyumba za kuishi Bopar Enterprises, Jiwe la msingi Salaam Cane Restaurant-K/Dimbani.

Miradi mingine itakayozinduliwa ni mradi wa mabweni mapya -Hasnu Makame Sekondari-Kibuteni ,jiwe la msingi jengo la maendeleo Kibuteni na uzinduzi wa hoteli la kitalii ya Johari-K Mkunguni.

Akielezea zaidi amesema pia kupitia tamasha hilo wanatangaza fursa za uwekezaji, vivutio vya utalii pamoja na kuhifadhi na kuenzi utamaduni wa Kizimkazi.

Ametumia nafasi hiyo kuelezea kupitia tamasha hilo manufaa yanayopatikana ni kuvutia uwekezaji, kuongeza watalii, ajira, biashara, mapato ya wananchi na Serikali, na kuchangia uchumi wa Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

“Tunawakaribisha wawekezaji, wadau wa utalii, tour operators, tour guides, travel agencies, wadhamini, vyombo vya habari, wasanii, watu mashuhuri na wadau wa maendeleo kushiriki Kizimkazi Festival ili kujionea fursa na kushiriki kuitangaza Kizimkazi duniani.”

Mwenyekiti huyo wa maandalizi tamasha la Kizimkazi amesema ujumbe mkuu katika tamasha hilo inasema Kizimkazi Festival si tamasha la burudani pekee; ni jukwaa la maendeleo linalounganisha utamaduni, utalii na uwekezaji kwa manufaa ya Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

“Karibuni Kizimkazi Festival mshuhudie utajiri wa utamaduni wetu, mjionee fursa za uwekezaji na vivutio vya utalii, na muwe sehemu ya safari ya kuijenga Kizimkazi kuwa kitovu cha maendeleo.”




Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma, Alimwoni Chaula amepongeza ushiriki wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba, 2026 akieleza kuwa maonesho hayo ni jukwaa muhimu la kulitangaza jiji na fursa zake kwa wananchi na wawekezaji.

Alitoa pongezi hizo alipotembelea banda la Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwenye maonesho hayo yanayoendelea jijini Dar es Salaam, ambapo alipata nafasi ya kuelezwa huduma zinazotolewa, maeneo ya uwekezaji pamoja na fursa mbalimbali zinazopatikana ndani ya Jiji la Dodoma.

Chaula alisema kuwa ameridhishwa na ushiriki wa jiji katika maonesho hayo na kusisitiza umuhimu wa kutumia kikamilifu nafasi hiyo kujitangaza ili wananchi wanaotembelea banda hilo waweze kufahamu na kuvutiwa na fursa zilizopo ndani ya Jiji la Dodoma.

"Ni vizuri mkatumia maonesho haya kujitangaza kikamilifu, kueleza kwa uwazi huduma mnazotoa, maeneo ya uwekezaji na fursa mbalimbali zilizopo ndani ya jiji letu ili wananchi na wadau wanaotembelea banda hili waone umuhimu wa kuchangamkia fursa hizo" alisema Chaula.

Aidha, alisisitiza kuwa ushiriki wa Jiji la Dodoma katika Maonesho ya Sabasaba unapaswa kuwa chachu ya kuhamasisha uwekezaji, kukuza biashara na kutangaza vivutio pamoja na huduma zinazotolewa na halmashauri kwa lengo la kuchochea maendeleo ya kiuchumi ya jiji hilo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Jiji la Dodoma, Dennis Gondwe alisema kuwa ushiriki wa jiji katika maonesho hayo unalenga kuitangaza Dodoma kama makao makuu ya nchi, kuonesha fursa za uwekezaji zilizopo, huduma za ardhi, biashara pamoja na miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa na halmashauri kwa manufaa ya wananchi na wawekezaji.

Maonesho ya 50 ya biashara ya Kimataifa Sabasaba, 2026 yanaendelea kuwa jukwaa muhimu kwa taasisi za umma na binafsi kuwasilisha huduma, bidhaa na fursa mbalimbali kwa wananchi huku yakitoa nafasi ya kubadilishana uzoefu na kuongeza uelewa kuhusu masuala ya maendeleo na uchumi.





Na John Mapepele, Wu hani - China

Serikali ya Tanzania imesisitiza dhamira yake ya kujenga sekta imara ya viwanda vya dawa na kuifanya nchi kuwa kitovu cha uzalishaji wa dawa kwa ukanda wa Afrika Mashariki na kwingineko barani Afrika, huku ikizidi kuvutia uwekezaji wa kimkakati kutoka China.

Akizungumza Julai 7,2026 katika kikao na viongozi wa kampuni ya Jointown Pharmaceutical Group nchini China, inayoongoza kwa uzalishaji wa madawa kwa upande wa makampuni binafsi nchini hapa, Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa amesema Tanzania imejipanga kuendeleza Eneo Maalum la Kiuchumi la Dawa na Vifaa Tiba la Mloganzila, ambalo litakuwa kitovu cha uwekezaji katika uzalishaji wa dawa, malighafi za dawa (APIs) na vifaa tiba.

Amesema, eneo hilo limeboreshwa kwa miundombinu ya kisasa na linaunganishwa kwa urahisi na Bandari ya Dar es Salaam pamoja na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere.

Waziri Mchengerwa amebainisha kuwa Serikali iko tayari kushirikiana na Jointown katika kuanzisha uzalishaji wa malighafi za dawa, hatua itakayoongeza uwezo wa Tanzania kujitosheleza kwa dawa muhimu na kuiwezesha kuhudumia masoko ya kikanda.

“Ushirikiano kati ya Jointown na Bohari ya Dawa (MSD) unatarajiwa kuleta mageuzi katika mifumo ya ugavi, uhifadhi na usambazaji wa dawa nchini kupitia matumizi ya teknolojia na uzoefu wa kampuni hii kubwa hapa China katika usimamizi wa minyororo ya usambazaji duniani” amesema Mhe. Mchengerwa

Aidha Mhe. Mchengerwa amethibitisha Serikali inayoongozwa na Rais wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, inafuatilia kwa karibu uwekezaji wa dawa nchini na ameahidi ushirikiano wa Serikali kwa wawekezaji watakaochangia maendeleo ya sekta ya afya.

Katika kuonesha utayari wa Serikali, Waziri Mchengerwa amesema Tanzania ipo tayari kutenga maeneo ya kutosha kwa ajili ya uwekezaji wa uzalishaji wa malighafi za dawa, akieleza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya dhamira ya dhati ya kuharakisha uanzishwaji wa viwanda vya kisasa vitakavyozalisha dawa kwa matumizi ya ndani na kwa ajili ya soko la Afrika.








Top News