Farida Mangube Sikonge, Tabora

Mkuu wa Wilaya ya Sikonge Thomas Mnyinga amewataka wakazi wa wilaya hiyo kulinda na kuhifadhi misitu ya miombo, akieleza kuwa rasilimali hiyo imeanza kuwa kivutio muhimu cha utalii na inaweza kuchangia ukuaji wa uchumi wa eneo hilo.

Akizungumza katika Tamasha la Staff Tour 2026 lililofanyika ndani ya hifadhi ya msitu wa mazingira Itulu hills na kubebwa na kauli mbiu “Tunaungana, Tunaitunza, Tunaburudika na Miombo,” Mkuu huyo wa Wilaya alisema ni muhimu kwa jamii kubadili mtazamo na kuitunza misitu hiyo kwa manufaa ya sasa na vizazi vijavyo.

Alisema pamoja na umuhimu wa miombo, bado kuna matumizi makubwa ya miti hiyo, hususan katika ukaushaji wa tumbaku ambapo wakulima hutumia kuni kwa wingi.

“Serikali ipo katika mpango wa kuleta mbadala wa kukaushia tumbaku ili kupunguza matumizi ya kuni na kulinda misitu yetu,” alisema.

Aliongeza kuwa uhifadhi wa misitu hiyo utasaidia kukuza utalii wa mazingira, ambao unaanza kujitokeza katika maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo.

Miongoni mwa vivutio vilivyotajwa ni Mto Koga, ambao unatenganisha mikoa ya Tabora na Katavi. Mto huo umeelezwa kuwa na uhai wa viumbe mbalimbali wakiwemo viboko wanaoonekana katika baadhi ya maeneo.

Aidha, ndege wa aina mbalimbali huonekana katika eneo la mto huo wakifika kutafuta chakula, hali inayoongeza mvuto kwa watalii wanaopenda kutazama wanyamapori na ndege.

Akizungumzia tamasha hilo, Afisa Utalii kutoka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Wilaya ya Sikonge Mhifadhi John Shayo alisema lengo ni kuhamasisha utalii wa miombo na kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa uhifadhi wa misitu hiyo yenye bioanuai kubwa.

“Tunataka jamii itambue kuwa misitu hii ina thamani zaidi ya matumizi ya kawaida, ikiwemo fursa za utalii,” alisema.

Mbali na shughuli za utalii wa asili, washiriki wa tamasha hilo pia walipata fursa ya kufurahia burudani mbalimbali zikiwemo ngoma za asili pamoja na vyakula mbalimbali ikiwemo nyama choma.

Tamasha hilo limeelezwa kuwa sehemu ya jitihada za kukuza utalii wa ndani huku likihamasisha uhifadhi wa rasilimali misitu katika Wilaya ya Sikonge.














Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma

Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi, amewasilisha bungeni mjini Dodoma makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Nishati kwa mwaka wa fedha 2026/2027, akieleza kuwa jumla ya Shilingi trilioni 2.525 zimetengwa kwa ajili ya utekelezaji wa majukumu ya wizara hiyo.

Akiwasilisha bajeti hiyo, Waziri Ndejembi amesema kati ya fedha hizo, Shilingi trilioni 2.462 sawa na asilimia 97.5 ya bajeti yote ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo. Kati ya fedha za maendeleo, Shilingi trilioni 1.602 ni fedha za ndani, huku Shilingi bilioni 859.9 zikiwa ni fedha kutoka nje ya nchi kwa ajili ya kugharamia miradi mbalimbali ya kimkakati katika sekta ya nishati.

Aidha, amesema jumla ya Shilingi bilioni 63.036 zimetengwa kwa ajili ya matumizi ya kawaida, sawa na asilimia 2.5 ya bajeti yote ya wizara. Kati ya fedha hizo, Shilingi bilioni 52.939 zimetengwa kwa ajili ya mishahara ya watumishi (PE), wakati Shilingi bilioni 10.097 zikitengwa kwa matumizi mengineyo ya kawaida (OC) kwa Wizara ya Nishati na taasisi zake, ikiwemo PURA.

Waziri Ndejembi alisisitiza kuwa bajeti hiyo inalenga kuimarisha upatikanaji wa nishati ya uhakika, kuendeleza miradi ya kimkakati na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa kupitia sekta ya nishati.


 

  

Meneja wa Ufungaji wa Mgodi wa Barrick Buzwagi, Mhandisi Zonnastral Mumbi, akizungumza katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.
Meneja wa Ufungaji wa Mgodi wa Barrick Buzwagi, Mhandisi Zonnastral Mumbi, akizungumza katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.
Meneja wa Ufungaji wa Mgodi wa Barrick Buzwagi, Mhandisi Zonnastral Mumbi, akizungumza katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.

Naibu Meya wa Manispaa ya Kahama na Diwani wa Kata ya Mwendakulima, Shabani Mikongoti, akizungumza katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.
Naibu Meya wa Manispaa ya Kahama na Diwani wa Kata ya Mwendakulima, Shabani Mikongoti, akizungumza katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.
Mkuu wa Shule ya Sekondari Mwendakulima, Bi. Neema Mfumya, akizungumza katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, yaliyofanyika Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.
Mkuu wa Shule ya Sekondari Mwendakulima, Bi. Neema Mfumya, akizungumza katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, yaliyofanyika Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.
Agnes Julius akisoma risala kwa niaba ya wahitimu katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.
Meneja wa Ufungaji wa Mgodi wa Barrick Buzwagi, Mhandisi Zonnastral Mumbi, akigawa vyeti kwa wahitimu katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, yaliyofanyika Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.
Meneja wa Ufungaji wa Mgodi wa Barrick Buzwagi, Mhandisi Zonnastral Mumbi, akiwa katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, yaliyofanyika Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.
Meneja wa Ufungaji wa Mgodi wa Barrick Buzwagi, Mhandisi Zonnastral Mumbi, akigawa vyeti kwa wahitimu katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, yaliyofanyika Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.
Wahitimu wakiwa katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.

*

Kampuni ya Barrick nchini yenye ubia na Serikali ya Tanzania kupitia kampuni ya Twiga Minerals imeeleza dhamira yake ya kuendelea kuunga mkono jitihada za Serikali katika kuhakikisha wanafunzi wanapata elimu bora katika mazingira salama na rafiki kwa kujifunzia.
Na Karama Kenyunko Michuzi Tv

CHU0 Cha Kodi (ITA) kimewakutanisha wadau mbalimbali wa ikiwemo sekta ya forodha, kodi na elimu kujadili namna ya kuandaa kozi ya uzamili katika forodha ili kukidhi uhitaji mkubwa wa wataalam na wabobezi wa forodha ndani na nje ya nchi.

Profesa. Isaya Jairo, mkuu wa Chuo hicho amesema hayo leo Aprili 22, 2026 jijini Dar es Salaam, wakati akifungua warsha ya siku moja ya mashauriano na wadau, wataalamu kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), wizara za serikali, taasisi za udhibiti, na taasisi za kitaaluma wamekutana kwa lengo la kuandaa mtaala unaozingatia umahiri (competency-based curriculum) unaoendana na viwango vya kitaifa, kikanda na kimataifa.

Amesema uongozi wa ITA umeomba wadau kushiriki kikamilifu katika mchakato wa kuandaa mtaala huo, akisisitiza kuwa utaalamu wao utahakikisha programu hiyo inakuwa ya vitendo, inayokidhi mahitaji ya soko, na endelevu katika kukidhi mahitaji ya sekta.

Prof. Jairo amesema programu hiyo inalenga kukabiliana na ongezeko la mahitaji ya utaalamu wa hali ya juu katika usimamizi wa forodha, hasa wakati mifumo ya biashara ya kimataifa inavyozidi kuwa changamano na kuendeshwa kwa teknolojia.

Ameibainisha kuwa mpango huo utawanufaisha moja kwa moja maofisa wa TRA na wataalamu wengine wanaohitaji uwezo wa hali ya juu wa uchambuzi na utekelezaji ili kukabiliana na changamoto zinazobadilika katika biashara.

Amesisitiza kuwa mtaala huo utaandaliwa kwa kuzingatia mfumo wa Elimu na Mafunzo kwa kuzingatia Umahiri (CBET) ili kuhakikisha wahitimu wanapata ujuzi wa vitendo unaohitajika katika mazingira halisi ya kazi.

Ameongeza kuwa mchango wa wadau ni muhimu katika kubainisha matokeo ya ujifunzaji yanayoakisi mahitaji halisi ya kiutendaji katika forodha na biashara ya kimataifa.

Aidha, programu hiyo itaendanishwa na taasisi za udhibiti na uhakiki wa ubora, ikiwemo Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET) na Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU), pamoja na wizara husika za kisera.

Amesisitiza umuhimu wa kuoanisha programu hiyo na mifumo ya kikanda na kimataifa ikiwemo Shirika la Forodha Duniani (WCO), Shirika la Biashara Duniani (WTO), Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), ili kuongeza ushindani wa kikanda na kuwezesha biashara.

Itakapotekelezwa, Shahada ya Uzamili katika Forodha na Biashara ya Kimataifa inatarajiwa kuwa ya kwanza ya aina yake nchini Tanzania na katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini.

Pia inatarajiwa kuziba pengo kubwa la ujuzi katika usimamizi wa forodha, uchambuzi wa sera za biashara, na usimamizi wa mapato.

Naye, Kisamo Mandali, afisa kutoka Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), amesema wataalamu wamekuwa wakikabiliana na shughuli ngumu za forodha kwa muda mrefu bila kuwa na njia maalum ya ndani ya kupata mafunzo ya juu.

Amesema pengo hilo sasa linashughulikiwa kupitia programu mpya iliyoundwa kujenga utaalamu wa hali ya juu na kuimarisha sekta hiyo.

Aliongeza kuwa mpango huo ni zaidi ya programu ya kitaaluma, bali ni uwekezaji wa muda mrefu katika uwezo wa taifa.

Pia alibainisha kuwa kuwashirikisha wadau tangu mwanzo kunaonesha dhamira thabiti ya kuandaa mtaala unaozingatia mahitaji halisi ya sekta.

Ummy Mmary kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ameonesha matumaini kama hayo, akisema mpango huo ni hatua iliyochelewa kwa muda mrefu, kwani wataalamu hawatalazimika tena kusafiri nje ya nchi kupata mafunzo maalum, huku utaalamu ukijengwa hapa nchini.

Kilichoanza kama mjadala sasa kinaanza kuchukua sura kama msingi wa mabadiliko—yanayotarajiwa kuandaa kizazi kipya cha wataalamu wa forodha na kubadilisha taswira ya biashara ya Tanzania










Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Serikali imesema itaendelea kuhakikisha upatikanaji wa uhakika wa mafuta nchini licha ya changamoto za kimataifa zinazoathiri mnyororo wa usambazaji wa nishati hiyo , ikiwemo vita inayoendelea katika Ukanda wa Mashariki ya Kati.

Akizungumza bungeni jijini Dodoma wakati wa uwasilishaji wa Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati kwa Mwaka wa Fedha 2026/27 ,Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Deogratius Ndejembi, alisema kuwa Serikali imeweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha wananchi wanapata bidhaa za mafuta ya petroli kwa uhakika.

“Sambamba na kuimarika kwa upatikanaji wa umeme, nchi yetu pia imeendelea kuwa na uhakika wa upatikanaji wa bidhaa za mafuta ya petroli licha ya changamoto za kimataifa zilizotokana na vita baina ya Marekani, Israel na Iran,” alisema Mhe. Ndejembi.

Alifafanua kuwa vita hiyo imesababisha athari kubwa katika usambazaji wa mafuta duniani, ikiwemo kufungwa kwa Mlango Bahari wa Hormuz ambao hupitisha zaidi ya asilimia 20 ya mafuta yote duniani, pamoja na kuathiri miundombinu ya uzalishaji na uhifadhi wa mafuta.

“Hali hii imeathiri kwa kiasi kikubwa nchi za Mashariki ya Kati ambako Tanzania inaagiza takribani asilimia 59 ya mafuta yake, huku asilimia 41 ikitoka India ambayo nayo hutegemea mafuta ghafi kutoka ukanda huo huo,” aliongeza.

Kutokana na hali hiyo, Waziri Ndejembi alisema Serikali imechukua hatua za haraka na za kimkakati ili kulinda usalama wa nishati nchini. Moja ya hatua hizo ni kuliwezesha Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kuagiza mafuta ya kutosha kwa kipindi cha miezi mitatu ijayo.

Aidha, alisema Serikali inaendelea kufuatilia kwa karibu mwenendo wa soko la mafuta duniani na iko tayari kuchukua hatua zaidi kulingana na mabadiliko yatakayotokea.



Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) limeendelea kuimarisha mikakati yake ya kuhakikisha usalama na huduma bora kwa watalii wanaotembelea hifadhi zake, hususan maeneo ya milima kama Kilimanjaro na Udzungwa.

Hatua hiyo imebainika wakati wa ufunguzi wa mafunzo maalum ya uokoaji, uhokozi na huduma ya kwanza kwa askari wa hifadhi, yaliyolenga kuwajengea uwezo wa kukabiliana na changamoto zinazoweza kuwakumba watalii wakiwa safarini.

Akifungua mafunzo hayo, Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi Kanda ya Mashariki, Fredrick Malisa, amesema TANAPA inaendelea kutoa mafunzo ya mara kwa mara kwa askari wake ili kuhakikisha wanakuwa tayari kukabiliana na hali yoyote ya dharura.

Amesema hifadhi za milima hupokea watalii wa aina mbalimbali wenye uwezo tofauti, hivyo ni muhimu kuwa na kikosi chenye ujuzi wa kuwahudumia haraka na kwa ufanisi bila kuongeza madhara kwa wahusika.

Kwa upande wake, Afisa Mhifadhi Mkuu kutoka hifadhi ya mlima kilimanjaro Miraji Mramba amesema askari kutoka Hifadhi ya Taifa Kilimanjaro wamefanya mafunzo hayo katika Hifadhi ya Taifa Udzungwa kwa lengo la kujifunza katika mazingira tofauti na kuongeza ufanisi wa kazi zao.

Amesema utaratibu huo wa mafunzo hufanyika kila mwaka, hasa wakati wa msimu wa watalii wachache, ili kujiandaa na msimu mkubwa wa wageni, huku akibainisha kuwa TANAPA itaendelea kusambaza elimu hiyo katika hifadhi nyingine zenye milima nchini.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Utalii katika Hifadhi ya Taifa Milima ya Udzungwa, Ahmed Nasori, amesema ujio wa mafunzo hayo ni fursa muhimu kwa askari wa hifadhi hiyo kujifunza na kubadilishana uzoefu na wenzao wa Kilimanjaro.

Amesema mazingira ya Udzungwa yanafanana kwa kiasi kikubwa na yale ya Kilimanjaro, hivyo mafunzo hayo yataongeza uelewa wa namna bora ya kukabiliana na changamoto za uokoaji katika maeneo ya milima.

Aliongeza kuwa hifadhi hiyo pia imekuwa kivutio kikubwa cha utalii, ikitoa fursa za shughuli mbalimbali kama kupanda milima, matembezi ya asili (hiking) na utalii wa picha, huku idadi ya watalii ikiendelea kuongezeka mwaka hadi mwaka.




Serikali kupitia Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imeendelea kuimarisha usimamizi na udhibiti wa shughuli za bidhaa za mafuta ya petroli nchini, hatua inayolenga kuhakikisha upatikanaji wa uhakika wa nishati, usalama wa miundombinu pamoja na ubora wa huduma kwa wananchi.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi, wakati akiwasilisha Hotuba ya Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 leo Aprili 22,2026 bungeni Dodoma.

Akieleza mafanikio ya utekelezaji huo hadi Machi 2026, EWURA imefanikiwa kutoa jumla ya leseni 636 kwa biashara mbalimbali katika sekta ndogo ya mafuta na gesi. Leseni hizo zinahusisha vituo vya mafuta mijini na vijijini, maghala ya kuhifadhia mafuta, pamoja na biashara ya usambazaji na uuzaji wa gesi ya kupikia (LPG) na vilainishi.

"Takwimu zinaonesha kuwa vituo vya mafuta mijini vimeongoza kwa kupata leseni nyingi zaidi, huku pia juhudi zikielekezwa katika maeneo ya vijijini ili kupanua huduma na kuongeza upatikanaji wa nishati kwa wananchi wa maeneo hayo. Hatua hii inaakisi mkakati wa Serikali wa kuhakikisha huduma za mafuta zinawafikia wananchi wote bila kujali maeneo yao."amesema Mhe.Ndejembi

Katika kuimarisha miundombinu ya sekta hiyo, EWURA pia ilitoa vibali 288 vya ujenzi wa miundombinu ya mafuta, ambapo vibali 137 vilihusu maeneo ya mijini na 143 vijijini. Vibali vingine vilihusisha maghala ya kuhifadhi mafuta na gesi, pamoja na miundombinu ya matumizi ya viwandani na migodini.

Sambamba na utoaji wa leseni na vibali, EWURA imeendelea kusimamia kwa karibu taratibu za uagizaji na usambazaji wa mafuta nchini. Katika ukaguzi wa ubora wa bidhaa, jumla ya sampuli 648 zilipimwa, ambapo sampuli 608 sawa na asilimia 93.83 zilikidhi viwango vinavyotakiwa. Vituo 22 vilivyobainika kuuza mafuta yasiyokidhi viwango vilichukuliwa hatua za kisheria, ikiwemo kufungiwa na kutozwa faini.

Aidha, ukaguzi wa miundombinu ya mafuta ulifanyika katika vituo 544, ambapo asilimia 86.95 ya miundombinu hiyo ilikidhi viwango vya ubora, ikiwa ni pamoja na masuala ya afya, usalama na mazingira. Wamiliki wa vituo 95 ambavyo havikukidhi vigezo walielekezwa kufanya maboresho ili kuendana na viwango vilivyowekwa.

Kwa ujumla, hatua hizi zinaonesha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha sekta ya mafuta inakuwa salama, yenye ufanisi na inachangia kikamilifu katika ukuaji wa uchumi wa Taifa, huku ikilinda maslahi ya watumiaji na mazingira.




NAIBU Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), amesema kuwa Serikali inatekeleza mkakati wa Mfumo wa Kodi ya Makadirio (Presumptive Tax Scheme) ili kuwahamasisha walipakodi wadogo wasiokuwa na kumbukumbu sahihi za mapato kusajili biashara zao na kuanza kulipa kodi kwa hiari.

Ameyasema hayo bungeni jijini Dodoma, wakati akijibu swali la Mbunge wa Busokelo Mhe. Lutengano Mwalwiba, aliyetaka kujua mpango wa Serikali wa kuweka vivutio maalum vya kikodi kwa Vijana wanaoanza biashara ili kuchochea ajira na kukuza uchumi.

Mhandisi Munde, alisema kuwa, mkakati huo unaolenga kuwasaidia walipakodi wadogo wasiokuwa na kumbukumbu sahihi za mapato au vitabu vya hesabu, kwa kuwa masharti yake ni mepesi na yanatabirika.

“Serikali pia imeanzisha utaratibu wa kipindi cha neema (grace period) kinachowaruhusu wafanyabiashara wapya kufanya biashara bila kulipa kodi kwa muda wa miezi sita tangu kuanza shughuli zao ili kutoa nafasi kwa wajasiriamali kukuza biashara zao na kujiimarisha kabla ya kuanza kulipa kodi”, alisema Mhandisi Munde.

Alisema kuwa Serikali inatambua umuhimu wa kutoa vivutio maalum vya kikodi kwa vijana ili kuchochea uanzishaji wa biashara na ajira, ikiwemo msamaha wa kodi na viwango pungufu, huku ikiendelea kufanya tathmini ya athari zake ili kuhakikisha usawa, ufanisi wa sera, na uendelevu wa mapato ya Serikali.

Kupitia Sheria ya Fedha ya Mwaka 2023 na Maboresho ya Mwaka 2024, Serikali pia imetoa ahirisho la kodi ya mapato (Corporate Income Tax) kwa kipindi cha miezi sita ya mwanzo kwa biashara mpya (start-ups), hatua inayolenga kusaidia biashara changa kukua na hatimaye kuwa na walipakodi wakubwa na endelevu.
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), akijibu swali la Mbunge wa Busokelo Mhe. Lutengano George Mwalwiba, aliyetaka kujua mpango wa Serikali wa kuweka vivutio maalum vya kikodi kwa Vijana wanaoanza biashara ili kuchochea ajira na kukuza uchum.
(Picha na Kitengo cha Mawasilino Serikalini, Wizara ya Fedha)


Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) akiagana na Kiongozi wa ujumbe wa Benki ya Exim ya China ambaye ni Naibu Meneja Mkuu wa Benki hiyo Bi. Liu Fang, baada ya mkutano kati yao kuhusu ushirikiano wa maendeleo, uliofanyika Ofisi za Wizara ya Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.

Kiongozi wa Ujumbe wa Benki ya Exim ya China ambaye ni Naibu Meneja Mkuu, wa Benki hiyo Bi. Liu Fang akitoa ahadi ya kuendeleza ushirikiano na Tanzania ili kufanikisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo wakati wa Mkutano na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), katika Ofisi za Wizara ya Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.

Na. Peter Haule na. Josephine Majura. WF. Dodoma

TANZANIA inaendelea kunufaika na miradi mikubwa ya mikopo yenye masharti nafuu inayotolewa kupitia Benki ya Exim ya China ikiwa ni pamoja na Mradi wa Njia ya Kusafirisha Umeme ya Kilovolti (kV) 400 Kaskazini-Mashariki (Dar es Salaam–Arusha) na mradi Upanuzi wa Mawasiliano ya Mtandao wa Simu Vijijini (Awamu ya Kwanza).

Hayo yamebainishwa jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) wakati wa mkutano na ujumbe wa Benki ya Exim ya China ulioongozwa na Naibu Meneja Mkuu wa Benki hiyo, Bi. Liu Fang.

Mhe. Munde alisema kuwa Mradi wa Njia ya Kusafirisha Umeme Dar es Salaam–Arusha na Uboreshaji wa Mfumo wa umeme Awamu ya Kwanza una thamani ya Dola za Marekani milioni 270.3 na Mradi wa Upanuzi wa Mawasiliano ya Mtandao wa Simu Vijijini Awamu ya Kwanza una thamani ya Dola za Marekani milioni 08.6.

“Miradi hii miwili inayoendelea yenye jumla ya thamani ya Dola za Marekani milioni 378.9, ambayo mikataba yake ilisainiwa tarehe 27 Septemba 2025, ni muhimu katika kuboresha uhakika wa upatikanaji wa umeme katika Gridi ya Taifa na kukuza ujumuishaji wa kidijitali katika maeneo ya vijijini”, alisema Mhe. Munde.

Vile vile Mhe. Munde alisema kuwa Wizara ya Fedha kwa kushirikiana na Benki ya Exim ya China kwa sasa iko katika hatua za mwisho za majadiliano kuhusu Rasimu ya Mkataba wa Mkopo wa masharti nafuu kwa ajili ya kugharamia Mradi wa Uanzishaji wa Vyuo vinne vya Ufundi Stadi (TVET) katika maeneo ya Zanzibar, Kigoma, Mtwara na Mwanza (Awamu ya Kwanza).

Alisema kuwa Mpango huo unatarajiwa kuongeza kwa kiasi kikubwa uwezo wa elimu ya ufundi na mafunzo ya stadi za kazi nchini na hivyo kuchangia katika maendeleo ya ujuzi na ajira kwa vijana.

Pia ameitaka Benki ya Exim ya China kuangalia namna ya kusaidia upatikanaji wa fedha kwa ajili ya mradi wa Umeme wa kV 400 Chalinze Segera, kV 220 Segera Tanga na njia ya umeme ya Chalinze - Bagamoyo na vituo vyake na Mtandao wa Mawasiliano Vijijini Awamu ya Pili.

Aidha Mhe. Munde alifikisha salamu na shukrani kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akieleza kuthamini ushirikiano wa muda mrefu uliopo kati ya Tanzania na China.

Alitoa shukrani za dhati kwa Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China kwa kuendelea kutoa msaada unaoendana kwa karibu na vipaumbele vya maendeleo ya Taifa vilivyoainishwa katika Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (2021/22–2025/26) pamoja na Dira ya Maendeleo ya Tanzania 2025.

Kwa upande wake Kiongozi wa ujumbe wa Benki ya Exim ya China na Naibu Meneja Mkuu, wa Benki hiyo Bi. Liu Fang alisema kuwa Benki yake itaendelea kushirikiana na Tanzania katika maeneo ya vipaumbele vitakavyowezesha kuchochea maendeleo na kutimiza malengo ya Dira 2050.

Aliyataja baadhi ya maeneo yatakayozingatiwa kuwa ni pamoja na miradi ya Nishati, Miundombinu ya Usafirishaji, TEHAMA na mengine ambayo itaongeza wigo wa maendeleo na kuimarisha ushirikiano kati ya pande hizo mbili.

Bi. Fang ameipongeza Tanzania kwa kupiga hatua kubwa katika maendeleo ya uchumi kwa kuwa si tu amesoma katika taarifa mbalimbali lakini pia ameshuhudia kaika ziara yake inayoendelea nchini Tanzania.

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) akieleza umuhimu wa ushirikiano kati ya Tanzania na Benki ya Exim ya China katika kufanikisha maendeleo ya pande hizo mbili, wakati wa mkutano na Ujumbe wa Benki hiyo ukiongozwa na Naibu Meneja Mkuu wa Benki hiyo Bi. Liu Fang, katika Ofisi za Wizara ya Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.


Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) na Kiongozi wa Ujumbe wa Benki ya Exim ya China ambaye ni Naibu Meneja Mkuu wa Benki hiyo, Bi. Liu Fang wakiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa pande hizo mbili, baada ya mkutano kuhusu ushirikiano wa maendeleo, uliofanyika Ofisi za Wizara ya Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.
(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha)
JESHI la Polisi linaendelea na uchunguzi wa kina kufuatia taarifa iliyochapishwa na kusambazwa katika mitandao ya kijamii na Hilda Newton tarehe 10 Aprili 2026, ikidai kuwa Serikali imepanga kumuua Mbunge Tundu Lissu kwa risasi.

Kwa mujibu wa taarifa rasmi iliyotolewa na Msemaji wa Jeshi la Polisi, uchunguzi huo unalenga kubaini ukweli wa madai hayo pamoja na kukusanya ushahidi utakaosaidia hatua za kisheria kuchukuliwa.

Katika hatua ya kukamilisha uchunguzi huo, Jeshi la Polisi limemuelekeza Hilda Newton kufika katika Ofisi ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) iliyopo katika Jengo la Makao Makuu Ndogo ya Polisi, Mtaa wa Ohio jijini Dar es Salaam, tarehe 24 Aprili 2026 saa nne asubuhi.

Polisi wamesema kuwa lengo la kumuita ni kumpa fursa ya kuwasilisha ushahidi alioudai kuwa anao, ili kusaidia uchunguzi unaoendelea kufanyika kwa mujibu wa sheria.

Hatua hiyo inafanyika kwa mujibu wa kifungu cha 11(2) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai, kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2023, kinachoruhusu mamlaka husika kumuita mtu yeyote mwenye taarifa muhimu katika uchunguzi wa jinai.

Jeshi la Polisi limewahimiza wananchi kutumia mitandao ya kijamii kwa uwajibikaji na kuepuka kusambaza taarifa zisizo na uthibitisho ambazo zinaweza kusababisha taharuki au kuvuruga amani ya nchi.
Katika hatua inayoashiria mwelekeo mpya wa soka la Tanzania, mdhamini mkuu wa Ligi Kuu ya NBC, Benki ya Taifa ya Biashara (NBC), kwa kushirikiana na Azam TV wamezindua rasmi kipindi kipya cha uchambuzi wa soka kiitwacho “Kona ya NBC”—jukwaa la kisasa litakalounganisha burudani, maarifa na fursa za kiuchumi kwa wadau wa mchezo huo.

Uzinduzi huo wa kihistoria ulifanyika jana jioni jijini Dar es Salaam, ukihusisha wadau mbalimbali wa soka akiwemo Mkurugenzi Mtendaji wa NBC, Theobald Sabi, Afisa Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi, Cornel Barnabas, Meneja wa Mahusiano ya Umma wa Azam Media, Christina Korosso, wachambuzi wa michezo, wanahabari pamoja na wachezaji wa zamani na wa sasa, wakiwakilishwa na kiungo mshambuliaji wa Azam FC, Nassor Saadun.

Hafla hiyo ilirushwa mubashara kupitia Azam TV, huku wageni wakipata fursa ya kuishuhudia kupitia skrini kubwa ndani ya ukumbi wa kisasa wa sinema wa Century Cinemax uliopo Mlimani City—taswira halisi ya namna teknolojia na burudani zinavyoungana kuleta uzoefu mpya kwa mashabiki.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa NBC, Theobald Sabi, alisisitiza kuwa uwekezaji wa benki hiyo kwenye soka unaenda mbali zaidi ya udhamini wa kawaida—unalenga kujenga mfumo endelevu wa kiuchumi unaonufaisha wadau wote wa mchezo huo.

“Kupitia ‘Kona ya NBC’, tunapanua wigo wa thamani katika soka—kuanzia kwa wachezaji, vilabu, vyombo vya habari hadi wafanyabiashara wadogo na wakubwa. Huu ni uwekezaji unaolenga ajira, ubunifu na ustawi wa vijana,” alisema Sabi.

Aliongeza kuwa tangu mwaka 2023, NBC imewekeza zaidi ya shilingi bilioni 32.6 katika maendeleo ya soka, ikiwa ni pamoja na udhamini wa Ligi Kuu ya NBC, ligi daraja la kwanza na ligi za vijana—hatua iliyochochea ushindani, uimara wa kifedha wa vilabu na kuongezeka kwa hamasa ya mashabiki.

Akionyesha matumaini yake, Sabi alitolea mfano wa mataifa makubwa ikiwemo Ujerumani ambao kupitia ligi yao maarufu ya Bundesliga ikiwa na dhana inayofahamika kama “football tractor effect”, soka limekuwa kichocheo kikubwa cha ukuaji uchumi likitumika kuvutia ukuaji wa sekta nyingine kama utalii, biashara, vyombo vya habari, na ajira.

“Lakini pia sote ni mashahidi jinsi ambavyo ligi Kuu ya Uingereza yaani English Premeier League inavyotumika kuimarisha uchumi wa nchi hiyo. Tumeona Ujerumani, tumeona Uingereza. Sasa ni wakati wa Tanzania. Yes, why not us?’’ alihoji Sabi.

Kwa upande wake, Meneja wa Mahusiano ya Umma wa Azam Media Christina Korosso alieleza kuwa ushirikiano huo ni hatua muhimu katika kuinua ubora wa maudhui ya michezo nchini.

“Kupitia ‘Kona ya NBC’, Azam TV tunaleta jukwaa la kisasa linalounganisha wadau wa soka—kuanzia uwanjani hadi majumbani. Lengo ni kuongeza ubora wa maudhui, ushiriki wa mashabiki na kukuza tasnia ya michezo kwa ujumla,” alisema.

Naye Afisa Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi, Cornel Barnabas aliipongeza NBC kwa mchango wake mkubwa katika mageuzi ya soka la Tanzania, akieleza kuwa uwekezaji huo unaendelea kufungua milango mipya ya fursa kwa vijana na kuimarisha nafasi ya soka katika uchumi wa taifa.

“Uwekezaji wa NBC unaendelea kuleta mageuzi makubwa katika soka letu. Sio tu unaongeza ushindani wa ligi, bali pia unafungua fursa kwa vijana na kuimarisha mchango wa soka katika uchumi wa taifa. Uzinduzi wa Kona ya NBC ni hatua muhimu katika kuendeleza mafanikio haya,” alisema Barnabas.

Kipindi cha “Kona ya NBC”, ambacho kitarushwa kupitia Azam Sports HD 1 kila Jumatatu saa 1:00 jioni na kurudiwa Jumanne, kinatarajiwa kuwafikia zaidi ya watazamaji milioni 14 kila wiki.

Kwa mujibu wa Mkuu wa Masoko wa Benki ya NBC, David Raymond, mbali na uchambuzi wa kina wa mechi, kipindi hicho kitajikita pia katika simulizi za mafanikio, majadiliano ya fursa za kiuchumi ndani ya michezo, pamoja na kuwapa mashabiki nafasi ya kushiriki na kutoa maoni yao.

“Kwa kuwa mpira wa miguu ni miongoni mwa burudani zinazopendwa zaidi nchini Tanzania, tunaamini kipindi hiki kinakwenda kutoa jukwaa madhubuti la kuifikia jamii kwa urahisi, huku kikitoa burudani na kuelimisha masuala ya kifedha.’’ Alibainisha Raymond.

Kwa mashabiki, hiki si kipindi cha kawaida—ni darasa jipya la kujifunza namna ya kunufaika na soka nje ya uwanja. Baadhi yao wameeleza matarajio makubwa wakiamini kuwa jukwaa hili litavunja dhana ya muda mrefu ya kushabikia bila kunufaika.

“Hiki ni kipindi kitakachotufungua macho. Kwa muda mrefu tumekuwa mashabiki tu, sasa tunakwenda kujifunza namna ya kunufaika kiuchumi kupitia mchezo tunaoupenda,” alisema Shabiki wa Yanga SC maarufu kwa jina la God Yanga kauli iliyoungwa mkono na mwenzake kutoka klabu hasimu ya Simba SC

Mkurugenzi Mtendaji wa NBC, Theobald Sabi (wa pili kushoto), akiwa na Afisa Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi, Cornel Barnabas (wa pili kulia), Meneja wa Mahusiano ya Umma wa Azam Media, Christina Korosso (katikati), Mkurugenzi wa Fedha wa NBC, Rayson Foya (kushoto), pamoja na Mkuu wa Mikakati wa NBC, Msafiri Shayo (kulia), wakionyesha baadhi ya taarifa muhimu kuhusu kipindi kipya cha uchambuzi wa soka “Kona ya NBC”. Kipindi hicho, kinachoandaliwa na mdhamini mkuu wa Ligi Kuu ya NBC—Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) kwa kushirikiana na Azam TV, kinalenga kuunganisha burudani, maarifa na fursa za kiuchumi kwa wadau wa soka nchini. Tukio hilo lilifanyika jana jioni jijini Dar es Salaam.




Akizungumza katika uzinduzi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa NBC, Theobald Sabi alisisitiza kuwa uwekezaji wa benki hiyo kwenye soka unaenda mbali zaidi ya udhamini wa kawaida—unalenga kujenga mfumo endelevu wa kiuchumi unaonufaisha wadau wote wa mchezo huo.

Akizungumza kwenye hafla hiyo, Afisa Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi, Cornel Barnabas aliipongeza NBC kwa mchango wake mkubwa katika mageuzi ya soka la Tanzania, akieleza kuwa uwekezaji huo unaendelea kufungua milango mipya ya fursa kwa vijana na kuimarisha nafasi ya soka katika uchumi wa taifa.

Kwa upande wake, Meneja wa Mahusiano ya Umma wa Azam Media Christina Korosso alieleza kuwa ushirikiano huo ni hatua muhimu katika kuinua ubora wa maudhui ya michezo nchini.


Hafla hiyo ilirushwa mubashara kupitia Azam TV, huku wageni wakipata fursa ya kuishuhudia kupitia skrini kubwa ndani ya ukumbi wa kisasa wa sinema wa Century Cinemax uliopo Mlimani City—taswira halisi ya namna teknolojia na burudani zinavyoungana kuleta uzoefu mpya kwa mashabiki


Uzinduzi huo wa kihistoria ulihusisha wadau mbalimbali wa soka akiwemo wachambuzi wa michezo, wanahabari pamoja na wachezaji wa zamani na wa sasa.


Mkuu wa Idara ya Mawasiliano na Mahusiano ya Umma wa Benki ya NBC Bw Godwin Semunyu (kushoto) akimpongeza mmoja wa waandaaji wa show hiyo mpya, Gabriel Hugo ambae pia ni Msimaizi wa udhamini wa Ligi Kuu ya NBC kutoka Benki ya NBC. Katikati ni Mkurugenzi wa Fedha wa NBC, Rayson Foya.



Uzinduzi huo wa kihistoria ulifanyika jana jioni jijini Dar es Salaam









Top News