Na. Saidina Msangi, WF, Abidjan, Côte d’Ivoire.

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mshamu Ali Munde (Mb), kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), ameongoza ujumbe wa Tanzania katika Mkutano wa Pamoja wa 9 wa Kamati Maalum ya Mawaziri (STC) ya Umoja wa Afrika inayoshughulikia Fedha, Uchumi, Mipango na Mtangamano, pamoja na Mkutano wa 5 wa Kamati ya Mawaziri wa Biashara, Utalii, Viwanda na Madini.

Mkutano huo wa kimkakati ulioanza rasmi tarehe 24 Julai 2026 jijini Abidjan, Côte d’Ivoire, unalenga kuweka misingi imara ya ushirikiano wa kiuchumi barani Afrika.

Mkutano huo umejadili kwa kina umuhimu wa nchi za Afrika kuharakisha juhudi za kuendeleza sekta ya viwanda kwa kuongeza thamani ya malighafi za ndani badala ya kusafirishwa zikiwa ghafi, kuimarisha minyororo ya thamani ya kikanda, pamoja na kuweka mazingira bora na wezeshi yatakayovutia uwekezaji wenye tija kiuchumi.

Wajumbe wa mkutano huo walibainisha kuwa, kutokana na Bara la Afrika kuwa na rasilimali nyingi za asili, ardhi kubwa yenye rutuba kwa ajili ya kilimo, madini ya kimkakati na idadi kubwa ya vijana ambao ndio nguvu kazi kubwa katika uzalishaji, kuna umuhimu kwa Afrika kuwa kama kitovu cha uzalishaji na biashara duniani.

Aidha, mkutano huo umehimiza umuhimu wa kuimarisha ukusanyaji wa mapato ya ndani, kuboresha usimamizi wa rasilimali za asili, na kupambana na ukwepaji kodi ili kukabiliana na pengo kubwa la ufadhili wa maendeleo ya miundombinu ya kisekta.

Mawaziri na wataalamu hao walikubaliana kwa pamoja kuwa maendeleo ya viwanda hayawezi kufikiwa bila uwepo wa mfumo imara wa kifedha utakaowezesha upatikanaji wa mitaji ya muda mrefu, kupunguza gharama za mikopo, na kuvutia sekta binafsi kushiriki kikamilifu katika miradi ya maendeleo.

Naibu Waziri wa Fedha, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), akifuatilia mada zilizokuwa zikijadiliwa katika Mkutano wa Pamoja wa 9 wa Kamati Maalum ya Mawaziri (STC) ya Umoja wa Afrika inayosimamia masuala ya Fedha, Uchumi, Mipango na Mtangamano pamoja na Mkutano wa 5 wa Kamati Maalum ya Mawaziri inayosimamia masuala ya Biashara, Utalii, Viwanda na Madini, jijini Abidjan, nchini Côte d’Ivoire.

Naibu Waziri wa Fedha, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), (katikati) Naibu Waziri wa Madini Mhe. Dkt. Steven Lemomo Kiruswa (kulia) na Naibu Waziri wa Viwanda, Mhe. Dennis L. Londo (kushoto), wakifuatilia mijadala katika Mkutano wa Pamoja wa 9 wa Kamati Maalum ya Mawaziri (STC) ya Umoja wa Afrika inayosimamia masuala ya Fedha, Uchumi, Mipango na Mtangamano pamoja na Mkutano wa 5 wa Kamati Maalum ya Mawaziri inayosimamia masuala ya Biashara, Utalii, Viwanda na Madini, jijini Abidjan, nchini Côte d’Ivoire.

Naibu Waziri wa Fedha, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), akiteta jambo na Naibu Katibu Mkuu Mtendaji, Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt. Blandina Kilama, katika Mkutano wa Pamoja wa 9 wa Kamati Maalum ya Mawaziri (STC) ya Umoja wa Afrika inayosimamia masuala ya Fedha, Uchumi, Mipango na Mtangamano pamoja na Mkutano wa 5 wa Kamati Maalum ya Mawaziri inayosimamia masuala ya Biashara, Utalii, Viwanda na Madini, jijini Abidjan, nchini Côte d’Ivoire.

Naibu Waziri wa Fedha, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), Naibu Katibu Mkuu Mtendaji, Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt. Blandina Kilama (wa pili kulia), na Kamishna Msaidizi Idara ya Fedha za Nje Wizara ya Fedha, Bw. James Msina (kushoto), wakimsikiliza Afisa Usimamizi Fedha Mkuu, Wizara ya Fedha, Bi. Glory Sindilo, akifafanua jambo katika Mkutano wa Pamoja wa 9 wa Kamati Maalum ya Mawaziri (STC) ya Umoja wa Afrika inayosimamia masuala ya Fedha, Uchumi, Mipango na Mtangamano pamoja na Mkutano wa 5 wa Kamati Maalum ya Mawaziri inayosimamia masuala ya Biashara, Utalii, Viwanda na Madini, jijini Abidjan, nchini Côte d’Ivoire.


Naibu Waziri wa Fedha, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), (katikati), Naibu Waziri wa Madini Mhe. Dkt. Steven Lemomo Kiruswa (kushoto) na Naibu Waziri wa Viwanda, Mhe. Dennis L. Londo (kulia), wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kufunguliwa kwa Mkutano wa Pamoja wa 9 wa Kamati Maalum ya Mawaziri (STC) ya Umoja wa Afrika inayosimamia masuala ya Fedha, Uchumi, Mipango na Mtangamano pamoja na Mkutano wa 5 wa Kamati Maalum ya Mawaziri inayosimamia masuala ya Biashara, Utalii, Viwanda na Madini, jijini Abidjan, nchini Côte d’Ivoire.

Naibu Waziri wa Fedha, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), (katikati), Naibu Waziri wa Madini Mhe. Dkt. Steven Lemomo Kiruswa (kushoto) na Naibu Waziri wa Viwanda, Mhe. Dennis L. Londo (kulia), wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kufunguliwa kwa Mkutano wa Pamoja wa 9 wa Kamati Maalum ya Mawaziri (STC) ya Umoja wa Afrika inayosimamia masuala ya Fedha, Uchumi, Mipango na Mtangamano pamoja na Mkutano wa 5 wa Kamati Maalum ya Mawaziri inayosimamia masuala ya Biashara, Utalii, Viwanda na Madini, jijini Abidjan, nchini Côte d’Ivoire. Kushoto ni Naibu Katibu Mkuu Mtendaji, Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt. Blandina Kilama, na kulia ni Naibu Gavana wa Sera za Kiuchumi na Fedha, Benki Kuu ya Tanzania, Dkt. Yamungu Kayandabila.




Naibu Waziri wa Fedha, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), akiteta jambo na Waziri wa Fedha wa Eswatini Mhe. Neal Rijkenberg, katika Mkutano wa Pamoja wa 9 wa Kamati Maalum ya Mawaziri (STC) ya Umoja wa Afrika inayosimamia masuala ya Fedha, Uchumi, Mipango na Mtangamano pamoja na Mkutano wa 5 wa Kamati Maalum ya Mawaziri inayosimamia masuala ya Biashara, Utalii, Viwanda na Madini, jijini Abidjan, nchini Côte d’Ivoire. Katikati ni Katibu wa Naibu Waziri wa Fedha, Bw. Yambi Kinyaki.





(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Abidjan, Côte d’Ivoire.)



NA MWANDISHI WETU, DAR

Mkandarasi anayetekeleza mradi wa Maduka ya Biashara ya Maria Nyerere (Maria Nyerere Shopping Mall) ulio chini Jumuiya ya Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT), amehimizwa kuongeza kasi ya ujenzi ili mradi huo ukamilike kwa wakati.

Wito huo umetolewa na Mwenyekiti wa UWT Taifa, Mary Chatanda, Julai 22, 2026, Jijini Dar es Salaam, katika ziara ya Wajumbe wa Kamati ya Utekelezaji ya Baraza Kuu la UWT Taifa, kukagua uhai wa Chama na miradi ya Jumuiya hiyo.

Chatanda amesema, ipo haja ya mkandarasi huyo kuongeza kasi ya ujenzi, huku akimshauri kuongeza wakandarasi wengine ili kumsaidia baadhi ya kazi na kuongeza kasi ya ujenzi wa mradi huo.

"Mradi unakwenda vizuri, isipokuwa kwa mwenendo unavyokwenda na kwa muda tuliokubaliana huenda asikamilishe kwa wakati. Mkandarasi tunachomuhitaji aukamilishe mradi kwa mujibu wa tulivyokubaliana na kama kuna maeneo yeye hana uwezo wa kufanya, akabidhi kwa wakandarasi wengine (sub contractors) ili kazi ikamilike kwa wakati," amesema Chatanda.

Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti UWT Taifa, Zainabu Shomari, amesema mradi huo ni utekelezaji wa maagizo ya Chama wa kuzitaka Jumuiya zake kuwa na vitega uchumi.

"Chama kimeelekeza Jumuiya zake kujitegemea kiuchumi, kwahiyo, mradi huu ni utekelezaji wa maagizo na Chama na kwa hakika UWT tutafanikiwa kujitegemea," amesema Shomari.

Ikumbukwe kuwa, mradi wa Maria Nyerere Shopping Mall unatekelezwa eneo la Gerezani Jijini Dar es Salaam, ambapo unategemewa kuongeza mapato ili Jumuiya  hiyo iwe na uwezo wa kuendesha shughuli zake bila kutegemea uwezeshwaji kutoka Chama ngazi ya Taifa.

Pamoja na mradi huo, Kamati hiyo, ilipata fursa ya kukagua eneo lake lenye ukubwa wa hekta 8.2, lililopo mtaa wa Zogo, kata ya Zingiziwa, wilayani Ilala, ambapo linategemewa kuongeza uwekezaji wa Jumuiya hiyo.









📍Awaonya wajumbe wasifanye ushabiki wa Messi na Ronaldo




Na Mashaka Mhando, Muheza.

MBUNGE wa Jimbo la Muheza ambaye pia ni Naibu Waziri wa Habari Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma 'MwanaFA', amewataka wajumbe wa Chama cha Mapinduzi (CCM) wilayani humo kutopepesa macho wala kubabaika linapokuja suala la kumchagua Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga katika uchaguzi mkuu wa chama hicho mwakani.

MwanaFA ametoa kauli hiyo Leo Julai 23 wakati akizungumza na Wana-CCM wa kata za Kwakifua na Tingeni, ambapo ametumia jukwaa hilo kumpigia debe zito Mwenyekiti wa sasa wa mkoa huo, Ustadh Rajab Abdallah, akieleza kuwa rekodi ya kazi zake za kukijenga chama haijawahi kufikiwa na kiongozi yeyote nchini.


Rekodi Zilizompa Kiki Ustadh Rajab


Akijenga hoja ya kwanini wajumbe hawapaswi kufanya makosa, Mhe. Mwinjuma aliwataka wanachama hao kutaja mwenyekiti yeyote nchini aliyewahi kujenga nyumba za watumishi wa chama kila wilaya, ambapo wajumbe walijibu "hakuna."

"Hebu nitajieni Mwenyekiti yeyote aliyejenga nyumba za watumishi wa chama mkoa wowote hapa nchini? Alihakikisha nyumba hizo zinakwisha kila wilaya. Wabunge tulikuwa tukichanga lakini Mwenyekiti alichanga zaidi. Hapa Muheza amehakikisha tunajenga ofisi ya wilaya ya kisasa ya ghorofa, huyu hapaswi kukosa kura hata moja ya Wana-Muheza," alisema MwanaFA.

Aliongeza kuwa kazi zinazofanywa na Mwenyekiti huyo zimerahisisha sana utekelezaji wa majukumu ya chama na kuwaondolea mzigo wabunge, hivyo kuwapa nafasi nzuri ya kubaki na jukumu moja tu la kuwahudumia wananchi.

"Nyumba za watumishi zimekamilika, jengo letu linakwenda kwa kasi, na juzi tena Mwenyekiti huyo huyo katoa Shilingi Milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa mwingine wa chama. Hatuwezi kupata mwenyekiti kama Ustadh Rajab. Huyu ni mtu wa kumshikilia na kwenda naye katika uchaguzi," alisisitiza.

"Hili Siyo Suala la Messi na Ronaldo, ni suala la uhai wa Chama chetu

Katika kusisitiza uzito wa jambo hilo, MwanaFA alitumia lugha ya kimichezo kuonya wajumbe wasichukulie uchaguzi huo kama ushabiki usio na tija.

"Tunatakiwa watu wote tujijue tutamuunga mkono nani. Hili siyo suala la kubishania nani mkali kati ya Messi na Ronaldo; hili ni suala linalogusa maisha yetu, uhai wa chama chetu na mustakabali wake kwa kuwa na mtu muhimu kama yeye.

"Kwa hiyo watu wote tuhakikishe tunamlinda, Mungu akimpa uhai Mwenyekiti wetu, tuhakikishe tunaendelea naye atuongozee chama ngazi ya mkoa tunamchagua tena," alionya MwanaFA.


Dua kwa Rais Samia

Mwisho, Mbunge huyo aliwaomba wananchi wa Muheza kuendelea kumsomea dua na kumuombea afya njema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Alisema Rais Samia ameutendea haki Mkoa wa Tanga na Wilaya ya Muheza kwa kupeleka fedha nyingi zilizowezesha utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati, ikiwemo ujenzi wa Hospitali ya Samia, miradi mikubwa ya maji, elimu, na miundombinu ya barabara.




Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi, leo Julai 23, 2026, ametembelea Pori la Akiba la Pande jijini Dar es Salaam na kukagua maendeleo ya miradi ya kuboresha miundombinu na huduma za utalii inayotekelezwa katika eneo hilo.

Miradi inayotekelezwa ni pamoja na ujenzi wa bwawa la kuogelea (swimming pool), bwawa la watoto (Kids Playing Grounds), uwanja mdogo wa mpira wa miguu na uwanja wa beach volleyball, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kupokea wageni na mashabiki wa AFCON 2027, ambayo Tanzania itaandaa kwa ushirikiano na Kenya na Uganda.

Dkt. Abbasi amesisitiza miradi hiyo ikamilike kwa wakati na kwa viwango vinavyotarajiwa ili kuhakikisha wageni watakaofika nchini wanapata fursa ya kutembelea na kufurahia vivutio vya utalii vilivyopo Pori la Akiba la Pande.

Pori la Akiba la Pande linapatikana takribani kilomita 45 kutoka katikati ya Jiji la Dar es Salaam na linaendelea kuimarishwa kuwa moja ya vivutio muhimu vya utalii wa asili nchini.












Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ameitaka Jumuiya ya Nchi za Afrika, Karibiani na Pasifiki (OACPS) kuhakikisha maazimio na matamko yanayopitishwa katika mikutano yake yanatekelezwa kupitia programu zenye manufaa ya moja kwa moja kwa nchi wanachama na wananchi.

Rais Dkt. Mwinyi ametoa wito huo leo, tarehe 23 Julai 2026, alipokutana na Katibu Mkuu wa OACPS, Mhe. Moussa Saleh Batraki na ujumbe wake , waliofika Ikulu Zanzibar.

Katika mazungumzo hayo, Rais Dkt. Mwinyi amesisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano katika maendeleo ya Uchumi wa Buluu, usimamizi endelevu wa rasilimali za bahari, uvuvi, uhifadhi wa mazingira ya bahari pamoja na kubadilishana uzoefu na teknolojia miongoni mwa nchi wanachama.

Ameeleza kuwa Zanzibar imeendelea kunufaika na programu mbalimbali zinazotekelezwa kupitia ushirikiano wa OACPS na Umoja wa Ulaya, zikiwemo programu zinazowawezesha wakulima wadogo kuboresha uzalishaji, kufikia viwango vya masoko na kuongeza ushindani wa mazao yao.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa OACPS, Mhe. Moussa Saleh Batraki, ameishukuru Tanzania kwa mchango wake katika shughuli za Jumuiya hiyo na kupongeza hatua zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuendeleza ajenda ya Uchumi wa Buluu. 

Halikadhalika, amesisitiza dhamira ya OACPS kuendelea kushirikiana na nchi wanachama katika kutafuta suluhisho la changamoto zinazokabili Mataifa Madogo ya Visiwa na kuimarisha maendeleo endelevu. 










Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Jeshi la Polisi Mkoa wa Dodoma linafanya uchunguzi wa tukio la mauaji ya Lea Eliud Mazengo (50), mkazi wa Kijiji cha Lamaiti wilayani Bahi, ambaye mwili wake ulipatikana ukiwa umefichwa shambani baada ya kutoweka kwa siku kadhaa.

Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa na familia, Lea aliondoka nyumbani Julai 20, 2026 kwenda shambani kwa ajili ya shughuli za kuvuna alizeti, lakini hakurejea nyumbani kama ilivyotarajiwa. Kutokana na kutopatikana kwake, ndugu pamoja na watoto wake walianza kumtafuta katika maeneo mbalimbali ya kijiji na mashambani.

Baada ya msako huo, mwili wa marehemu ulionekana ukiwa umefunikwa chini ya magunia ya alizeti yaliyokuwa shambani, hali iliyozua mshtuko mkubwa kwa familia na wakazi wa eneo hilo.

Akizungumza kuhusu tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, ACP Gallus Hyera, amesema uchunguzi wa awali unaonesha kuwa marehemu alifariki baada ya kukabwa shingoni. Amesema mtu anayehusishwa na tukio hilo ni aliyekuwa mume wake, huku chanzo kinachodaiwa kuchunguzwa kikitajwa kuwa ni wivu wa kimapenzi.

Mmoja wa wanafamilia ameeleza kuwa kabla ya tukio hilo, kulikuwa na migogoro ya kifamilia kati ya marehemu na mume wake, ikiwemo malalamiko yanayohusiana na mahitaji ya nyumbani na chakula. Aidha, amesema migogoro hiyo ilipelekea marehemu kuondolewa katika chumba walichokuwa wakilala na kuanza kutumia sebule kama sehemu yake ya kulala.

ACP Hyera amesema uchunguzi bado unaendelea ili kubaini mazingira yote yaliyopelekea kifo hicho na hatua zaidi za kisheria zitachukuliwa baada ya uchunguzi kukamilika.

Viongozi wa Kijiji cha Lamaiti wamemuelezea marehemu kuwa alikuwa kiongozi wa serikali ya kijiji na mwanajamii aliyekuwa akiheshimika kutokana na mchango wake katika shughuli za maendeleo ya kijiji. Tukio hilo limeacha simanzi kubwa kwa familia, viongozi na wakazi wa eneo hilo.



-Dkt. Numbi atoa somo kutoka Ghana kuhusu usimamizi wa ushirikishwaji wa wazawa katika Sekta ya Madini


📍MWANZA

Tume ya Madini imejipanga kuimarisha usimamizi wa ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini kwa kuhakikisha watoa huduma na wazalishaji wa bidhaa wanakidhi vigezo na viwango vya ubora vinavyohitajika, hatua inayolenga kuongeza mchango wa sekta hiyo katika ukuaji wa uchumi wa nchi.

Hayo yamesemwa leo, Julai 23, 2026, jijini Mwanza na Mwenyekiti wa Kamati ya Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini, Dkt. Theresia Numbi, kwenye Jukwaa la Tano la Utekelezaji wa Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini (LCCF 2026), linalowakutanisha wadau mbalimbali wa sekta hiyo.

Dkt. Numbi amesema Tume itaendelea kuboresha usimamizi wa eneo la ushirikishwaji wa Watanzania ili kuhakikisha wananchi wanapata fursa zaidi za kushiriki katika shughuli za uchimbaji wa madini, utoaji wa huduma, uzalishaji wa bidhaa na maeneo mengine ya mnyororo wa thamani wa Sekta ya Madini.

Akielezea uzoefu wa Ghana katika usimamizi wa ushirikishwaji wa wazawa, Dkt. Numbi amesema nchi hiyo imeweka mfumo madhubuti unaowataka waombaji wa fursa katika Sekta ya Madini kuwasilisha mipango ya ushirikishwaji wa wazawa, kulipa ada maalum na kurejesha sehemu ya fedha kwa Serikali kila mwisho wa mwaka.

Amesema mfumo huo pia unahakikisha watoa huduma wanakidhi vigezo vya kitaalamu na kuwa na uwezo unaohitajika kabla ya kupewa fursa ya kutoa huduma katika migodi ya madini.

Dkt. Numbi amewataka watoa huduma katika Sekta ya Madini kuhakikisha wanakidhi vigezo vinavyohitajika katika utoaji wa huduma na bidhaa migodini, sambamba na kuhakikisha bidhaa na huduma hizo zina ubora unaokidhi viwango vya juu.

“Ni muhimu kwa watoa huduma kuhakikisha wanakidhi vigezo vinavyohitajika na kutoa bidhaa na huduma zenye ubora unaokidhi viwango vya juu, kwa kuwa ubora ni msingi wa ushindani na uendelevu wa biashara katika Sekta ya Madini,” amesema Dkt. Numbi.

Aidha, amewataka Watanzania wanaoshiriki katika utoaji wa huduma na uzalishaji wa bidhaa kwa ajili ya migodi kuendelea kuimarisha uwezo wao, kuzingatia viwango vya ubora na kutumia teknolojia ili kuongeza ushindani na kunufaika zaidi na fursa zinazotokana na Sekta ya Madini.

Jukwaa hilo, ambalo leo limefikia siku yake ya pili, linaendelea kujadili masuala mbalimbali yanayolenga kuimarisha ushiriki wa Watanzania katika Sekta ya Madini, likiwemo suala la ushirikishwaji wa Watanzania katika Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGML), uzoefu bora kutoka kwa kampuni za Kitanzania zilizofanikiwa katika utekelezaji wa dhana ya ushirikishwaji wa Watanzania, pamoja na umuhimu wa kuzalisha rasilimaliwatu wenye ujuzi unaoendana na ukuaji wa teknolojia mpya katika Sekta ya Madini.

Vilevile, mdahalo maalum unajadili ajira, mafunzo na uhawilishaji wa teknolojia kama kichocheo cha kuongeza ushiriki na ujumuishaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini, sambamba na utekelezaji wa mipango ya urithishaji wa nafasi za kazi, changamoto zinazojitokeza na hatua zinazopaswa kuchukuliwa.

Jukwaa la LCCF 2026 limewakutanisha wadau mbalimbali wa Sekta ya Madini, wakiwemo makampuni ya uchimbaji wa madini, watoa huduma migodini, wafanyabiashara wa madini, wawekezaji, taasisi za umma na binafsi, pamoja na vyama vya wachimbaji wa madini nchini.

Jukwaa hilo linafanyika chini ya kaulimbiu: “Kutoka Majadiliano hadi Utekelezaji: Kujenga Sekta Imara ya Madini kupitia Ushirikishwaji wa Watanzania na Uanzishwaji wa Viwanda.”








Na Mwandishi Wetu

KATIKA kuunga mkono juhudi za Serikali za kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia, Oryx Gas Tanzania imetoa mafunzo ya matumizi salama na sahihi ya gesi ya kupikia kwa makundi ya wajasiriamali mbalimbali yakiwemo mama na baba lishe.

Mafunzo hayo yametolewa leo Julai 23,2026 katika Tamasha la Samaki Bagamoyo ambapo wajasiriamali zaidi ya 600 ambao wanashiriki tamasha hilo wamepatiwa mafunzo hayo kupitia maofisa wa Oryx Gas wakiongozwa na Meneja Mafunzo Peter Ndomba.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo Ndomba ametumia nafasi hiyo kuelezea amesema faida za kutumia LPG ikilinganishwa na nishati nyingine za kupikia, ikiwemo kupunguza gharama za uendeshaji, kuokoa muda wa kupika, kulinda afya kwa kupunguza moshi hatarishi, na kuhifadhi mazingira.

Pia amesema wajasiriamali na washiriki wa tamasha hilo wamejifunza mbinu bora za usalama zikiwemo ukaguzi wa mtungi, regulator na bomba kabla ya matumizi.

Nyingine ni namna ya kutambua uvujaji wa gesi na hatua sahihi za kuchukua,matumizi ya vifaa vilivyoidhinishwa na vyenye ubora,uhifadhi salama wa mitungi ya gesi, tahadhari za kuzuia ajali na hatua za kuchukua wakati wa dharura.

Aidha wamefundishwa mbinu bora za matumizi salama ya LPG katika shughuli za kila siku za upishi pamoja na athari za kuni na mkaa kwa mazingira na afya ya jamii hasa kwa kundi kubwa la wanawake ambao wanaathirika wa moshi wa kuni na mkaa kila siku.

“Kupitia mafunzo haya, Oryx Gas Tanzania inaendelea kuwawezesha wafanyabiashara wa chakula kutumia nishati safi kwa usalama, kuongeza ufanisi wa biashara zao na kuchangia afya bora pamoja na mazingira safi.

“Elimu ya matumizi salama ya LPG ni msingi wa kujenga jamii salama na kufanikisha ajenda ya taifa ya matumizi ya nishati safi ya kupikia.Oryx Gas Tanzania imekuwa kinara wa nishati safi na sasa imejikita pia kutoa elimu kwa makundi mchini Tanzaia ili kuhakikisha matumizi endelevu ya nishati safi.”











Top News