Na Mwandishi wa OMH

Kibaha, Pwani. Ofisi ya Msajili wa Hazina (OMH), kwa kushirikiana na Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), imeendesha mafunzo ya siku nne kwa watumishi wapya 20 walioajiriwa katika ofisi hiyo, kwa lengo la kuwajengea uwezo maalumu wa kiutendaji katika utumishi wa umma.

Mafunzo hayo ya siku nne yalifanyika katika Chuo cha Uongozi cha Mwalimu Nyerere kilichopo wilaya ya Kibaha, Mkoa wa Pwani, kuanzia Januari 13 hadi 16, 2026.

Mafunzo hayo yaliendeshwa na Mkurugenzi wa Utawala na usimamizi wa Rasilimali watu kutoka ofisi ya Msajili wa Hazina Bw. Chacha Marigiri, wakufunzi kutoka TPSC, wataalamu kutoka Hospitali ya Mnazi mmoja Pamoja na wataalaamu wa fedha na uwekezaji kutoka Mfuko wa Uwekezaji wa UTT AMIS.

Bw. Marigiri alitoa mafunzo kuhusu matumizi sahihi ya muda, akisisitiza umuhimu wa kuweka uwiano kati ya kazi na maisha binafsi ili kuepusha changamoto zinazoweza kumfanya mtumishi wa umma kushindwa kutekeleza majukumu yake.

“Watumishi wengi hushindwa kufanya kazi kwa ufanisi kwa sababu ya kukosa matumizi sahihi ya muda na kutoweka vipaumbele katika shughuli zao,” alisisitiza.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo kwa niaba ya Mkuu wa TPSC, Bw. Hosea George ambaye ni mhadhiri kutoka chuo hicho alisema mafunzo hayo ni muhimu na mahususi kwa watumishi wapya ili kuwajengea uwezo wa kufanya kazi kwa kuzingatia maadili ya utumishi wa umma.

“Mafunzo haya yanalenga kuchochea maendeleo ya serikali, pamoja na taasisi na mashirika ya umma yanayosimamiwa na Ofisi ya Msajili wa Hazina,” alisema Bw. George.

Miongoni mwa mada zilizofundishwa ni pamoja na maadili na utendaji katika utumishi wa umma, Muundo wa serikali ya jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na uendeshaji wa shughuli zake kwa Tanzania bara na Zanzibar, mapitio ya sheria mbalimbali za utumishi wa umma, elimu ya afya ya ukimwi na magonjwa yasiyoambukizwa, afya ya akili, kupima utenda kazi wa watumishi pamoja na elimu ya fedha na kuweka akiba.

Akizungumza wakati wa kutoa mada ya afya, Dkt. Frank Mlaguzi kutoka Hospitali ya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam aliwataka watumishi wa umma kuzingatia utunzaji wa afya zao dhidi ya magonjwa ya kuambukiza na yasiyoambukiza kama kisukari, shinikizo la damu, homa ya ini pamoja na changamoto za afya ya akili, akieleza kuwa magonjwa hayo huathiri kwa kiasi kikubwa utendaji kazi.

Bw. Chacha Marigiri aliwatunuku vyeti wahitimu wa mafunzo hayo na kukipongeza Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kwa kutoa mafunzo yenye tija, akibainisha kuwa mafunzo hayo yatasaidia kujenga watumishi wenye maadili, bidii na weledi.

Naye Goodluck Mtebene, mtumishi mpya wa umma katika Ofisi ya Msajili wa Hazina, Kurugenzi ya Fedha na Uhasibu, aliishukuru Ofisi ya Msajili wa Hazina pamoja na TPSC kwa kuandaa mafunzo hayo.

“Mafunzo haya yamekuwa mwongozo muhimu katika kuufahamu vyema utumishi wa umma. Tunaahidi kuyazingatia maadili yote tuliyofundishwa katika utekelezaji wa majukumu yetu,” alihitimisha.





 

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo imeipongeza Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) kwa utendaji kazi mzuri, maendeleo na mabadiliko makubwa yanayoonekana katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

Pongezi hizo zimetolewa , katika Ofisi za Bunge jijini Dodoma na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Deodatus Mwanyika (Mb), baada ya Kamati kupokea Taarifa ya Muundo na Majukumu ya BRELA iliyowasilishwa na Afisa Mtendaji Mkuu wa BRELA, Bw. Godfrey Nyaisa.

Mhe. Mwanyika amesema kuwa, licha ya kazi nzuri inayoendelea kufanywa na BRELA, bado kuna changamoto ya wafanyabiashara na wamiliki wa kampuni wengi kutohuisha taarifa za kampuni zao kupitia mfumo wa BRELA. Ameeleza kuwa tatizo hilo ni kubwa, lakini wananchi wengi hawalitambui ipasavyo.

“Hili tatizo ni kubwa lakini wengi hawalielewi; wengi wana kampuni lakini hawajahuisha taarifa za kampuni hizo,” amesema Mhe. Mwanyika.

Kutokana na hali hiyo, Mhe. Mwanyika ameielekeza Wizara ya Viwanda na Biashara kufanya utafiti na kutathmini namna ya kuboresha mfumo wa uhuishaji wa taarifa za biashara na kampuni, ili kuja na mfumo wezeshi, unaoongeza ufanisi na kuharakisha utoaji wa huduma.

Aidha, Mwenyekiti huyo amesisitiza umuhimu wa kuhuisha taarifa za biashara na kampuni, akitoa wito kwa wafanyabiashara kuchukua hatua hiyo kwa hiari na kwa wakati.

“Kuhuisha taarifa ni jambo jema, na ni muhimu tukalifanye,” amesisitiza.

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa BRELA, Bw. Godfrey Nyaisa, amesema kuwa Wakala itaendelea kutoa elimu kwa Waheshimiwa Wabunge kupitia Kamati hiyo ili kuwajengea uelewa mpana kuhusu majukumu ya BRELA pamoja na mifumo ya kidijitali inayotumika katika utoaji wa huduma.

Bw. Nyaisa ameeleza kuwa, pamoja na mafanikio yaliyopatikana, uelewa mdogo wa wananchi kuhusu matumizi ya mifumo ya kidijitali bado ni miongoni mwa changamoto zinazokwamisha urasimishaji wa biashara na utoaji wa leseni.

Amefafanua kuwa mfumo wa BRELA ni rafiki kwa mtumiaji na unajieleza wenyewe, hivyo kumwezesha mwananchi kujisajili moja kwa moja bila usumbufu.

“Mfumo wa BRELA ni rafiki kwa mtumiaji na unajieleza wenyewe, hivyo humwezesha mtu kuingia moja kwa moja na kusajili kampuni yake bila usumbufu,” amesema Bw. Nyaisa.

Ameongeza kuwa BRELA inaendelea kutoa elimu kwa wananchi ili kuwahamasisha kufahamu kuwa mchakato wa usajili wa biashara, kampuni na utoaji wa leseni si mgumu kama inavyodhaniwa.

Amebainisha kuwa katika mapitio ya sheria yanayoendelea, BRELA inapendekeza kutambuliwa rasmi kwa Mawakala wa Usajili wa Kampuni, ili kusaidia wananchi wanaokutana na changamoto wakati wa usajili.

“Lengo ni kuhakikisha mwananchi akikwama, anapata msaada kutoka kwa watu wanaotambulika na kuaminika,” amesisitiza Bw. Nyaisa.

Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Januari 17, 2026 ameongoza kikao cha kazi kuhusu ujenzi wa miradi ya barabara za haraka (Express Ways) kwa ubia kupitia mfumo wa PPP.

Kikao hicho kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Waziri Mkuu, kimehudhuriwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, William Lukuvi, Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, Naibu Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile.

Wengine ni Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. James Kilabuko, Katibu Mkuu Wizara ya Uchukuzi, Prof. Godius Kahyarara pamoja na watendaji wa Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Binafsi (PPPC), wakiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji, David Kafulila.



KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Balozi Dkt.Asha-Rose Migiro akiwa ameambatana na Naibu Katibu Mkuu Bara Ndugu John Mongella,leo Januari 17,2026 amekagua maendeleo ya mradi wa ujenzi wa Ofisi ya Makao Makuu ya Chama hicho katika eneo la NCC jijini Dodoma.


Taasisi ya Rotaract Club of Young Professionals Tanzania leo imetoa msaada wa viti na meza za kusomea pamoja na kichomea taka kwa wanafunzi wa Shule ya Msingi Toa Ngoma, hatua inayolenga kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia shuleni hapo.

Akizungumza mara baada ya kukabidhi vifaa hivyo, mwakilishi wa taasisi hiyo Glory Mwankenja amesema msaada huo wenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 3.5 za Kitanzania unalenga kuwasaidia wanafunzi kwa ujumla, hususan wale wenye changamoto za uoni, ili waweze kusoma katika mazingira salama, rafiki na yenye motisha.

Mwankenja ameongeza kuwa Rotaract inaamini elimu bora huanzia na mazingira bora, hivyo wameamua kushirikiana na jamii kusaidia shule zinazokabiliwa na changamoto za miundombinu na vifaa vya msingi vya kujifunzia.

Aidha, uongozi wa shule hiyo umeushukuru uongozi wa Rotaract kwa msaada huo, wakisema utapunguza uhaba wa samani darasani na kuongeza usafi wa mazingira kwa kuwepo kwa kichomea taka, jambo litakalosaidia kulinda afya za wanafunzi.

Rotaract ni jumuiya ya vijana wataalamu inayofanya kazi chini ya mwamvuli wa Rotary International, ikilenga kuwajenga vijana kupitia huduma kwa jamii, uongozi na maendeleo ya taaluma.

Nchini Tanzania, Rotaract Club of Young Professionals Tanzania imekuwa mstari wa mbele kushiriki katika miradi ya kijamii kama elimu, afya, mazingira na uwezeshaji wa vijana, kwa lengo la kuleta mabadiliko chanya katika jamii na kukuza uzalendo wa kushiriki maendeleo.

Kupitia miradi kama huu wa Shule ya Msingi Toa Ngoma, Rotaract inaendelea kuthibitisha dhamira yake ya kuunganisha taaluma na huduma kwa jamii kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.





Balozi wa Tanzania nchini Sweden, Mhe. Mobhare Matinyi akielezea vivutio vya utalii vya Tanzania pamoja na filamu ya Tanzania: The Royal Tour, wakati wa Maonesho ya Utalii ya Kimataifa ya Matka, yanayoendelea jijini Helsinki, Finland.

UBALOZI wa Tanzania nchini Sweden umeratibu na kushiriki katika Maonesho ya Kimataifa ya Utalii ya Matka yanayofanyika jijini Helsinki, Finland, kuanzia tarehe 14-18 Januari, 2026, huku ukitangaza vivutio vya utalii vya Tanzania pamoja na filamu ya Tanzania: The Royal Tour.

Maonesho hayo ni miongoni mwa maonesho makubwa barani Ulaya yakijumuisha kampuni 950 za utalii, usafiri wa ndege, vyombo vya habari, na ushauri elekezi wa utalii kutoka duniani kote ambapo katika siku ya kwanza yalipokea washiriki 56,000 wakiwemo watalii watarajiwa.

Kampuni binafsi za Lifestyle Safaris & Holidays na Lifetime Safaris za Tanzania nazo zinashiriki katika maonesho hayo zikiwa na timu ya Ubalozi wa Tanzania. Nchi zingine za Afrika zinazoshiriki ni Uganda, Kenya, Ushelisheli, Namibia, Afrika Kusini, Senegal, Moroko, Tunisia na Misri.

Balozi wa Tanzania nchini Sweden, Mhe. Mobhare Matinyi, anayeiwakilishia pia Tanzania katika nchi za Nodiki, Baltiki na Ukraina, alitumia jukwaa kuelezea namna Tanzania ilivyopata heshima kubwa ya kushinda Tuzo za Utalii za Dunia tarehe 6 Desemba 2025, nchini Bahrain, ikiwa ni mwaka wa tatu mfululizo.

Balozi Matinyi alielezea pia namna Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, alivyoshiriki na kuigiza katika filamu ya kuitangaza Tanzania ya dakika 57 iitwayo Tanzania: The Royal Tour akiwa na mwandishi wa Marekani mshindi wa Tuzo ya Emmy, Peter Greenberg, mwaka 2022.

Balozi Matinyi aliiambia hadhira kwamba Tanzania ina vivutio vitatu kati ya Maajabu Saba ya Asili ya Afrika na pia maeneo saba yanayotambuliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) kama Urithi wa Dunia, akiutaja mathalani Mlima Kilimanjaro, uhamaji mkubwa wa wanyamapori hifadhini Serengeti na bonde la Ngorongoro. Mbali ya hifadhi za taifa 22, Balozi Matinyi pia alitaja utajiri wa utamaduni wa makabila 126 ya Tanzania, hifadhi za historia ya kale kama michoro ya mapangoni ya Kondoa, Mji Mkongwe wa Zanzibar na miji ya Bagamoyo na Kilwa.

Balozi Matinyi pia alitumia maonesho hayo kufanya mazungumzo na wadau mbalimbali wakiwemo Afisa Mtendaji Mkuu wa Atlantic Link, Bi. Karin Gert Nielsen na Mwakilishi wa Danish Travel Show, zote za Denmark, Bw. Johnny Frandsen; Meneja wa kampuni ya Flygresor ya Sweden, Bw. Peter Hallgren; na kwa kampuni za Finland Mwanzilishi na Mkurugenzi Mwendeshaji wa GapEdu, Bw. Jyrki Nilson; Mkurugenzi Mwendeshaji wa Amanihoiva Limited, Bw. Juha Valtanen na Mwakilishi wa Matka Travel Fair, Inkeri Vainik. Mazungumzo hayo yalilenga namna ya kushirikiana katika kuutangaza zaidi utalii wa Tanzania barani Ulaya.

Imetolewa na:
Ubalozi wa Tanzani nchini Sweden,
17 Januari, 2025.
Balozi wa Tanzania nchini Sweden, Mhe. Mobhare Matinyi, akizungumza na Mkurugenzi Mwendeshaji wa kampuni ya GapEdu ya Finland, Bw. Jyrki Nilson, kwenye banda la Tanzania wakati wa Maonesho ya Utalii ya Kimataifa ya Matka, yanayoendelea jijini Helsinki, Finland.
Balozi wa Tanzania nchini Sweden, Mhe. Mobhare Matinyi (kulia) pamoja na Afisa Ubalozi Abel Maganya, wakizungumza na Bw. Peter Hallgren wa kampuni ya Flygresor ya Sweden kwenye banda la Tanzania wakati wa Maonesho ya Utalii ya Kimataifa ya Matka, yanayoendelea jijini Helsinki, Finland.
Mbunge wa Jimbo la Mtumba Mh. Anthony Mavunde kwa kushirikiana na wananchi wa eneo la ya Ngayagaye kata ya Ipala wameanzisha ujenzi wa madarasa ya shule ya Msingi ili kuwapunguzia mwendo watoto wanaotembea umbali mrefu kufuata shule.

Uanzishwaji wa ujenzi wa Shule hii ni utekelezaji wa ahadi ya Mh. Mavunde aliyoitoa tarehe 21.09. 2025 wakati wa Kampeni ya Uchaguzi Mkuu ambapo aliahidi kuanzisha ujenzi wa Shule hiyo na baadaye kuiomba Serikali kuunga mkono jitahada hizo.

“Ni dhamira ya serikali yetu kuona watoto wetu hawatembei umbali mrefu kufuata shule ndio maana leo tupo hapa kuanzisha ujenzi wa darasa la awali ili tuwapunguzie mwendo watoto wetu.

Serikali chini ya Rais Dkt. Samia S. Hassan imefanya kazi kubwa ya ujenzi wa miundombinu ya madarasa na ninaamini hata hapa itatuunga mkono juhudi hizi za wananchi.

Tutahakikisha ujenzj huu unachukua muda mfupi kukamilika kwa madarasa ili watoto hawa wapate elimu yao hapa hapa” Alisema Mavunde

Aidha wakati huo huo Mbunge Mbunge amekabidhi Matofali 2000,saruji mifuko 50,Baiskeli 20 na Bajaj kubwa mbili zenye uwezo wa kubeba watoto 20 ambazo zitasaidia usafiri wa watoto hao mpaka madarasa yatakapokamilika.

Wakitoa shukrani zao Madiwani wa Kata za Ipala na Hombolo Makulu Mh. Andrea Muhulo na Mh. Mokiwa Sahali wamemshukuru Mbunge Mavunde kwa kutimiza ahadi yake ya uanzishwaji wa ujenzi wa shule na hivyo kuwataka wananchi wa eneo hilo kujitokeza kwa wingi kuunga mkono jitahidi za Mbunge katika kufanikisha ujenzi huo.





📌Wakandarasi wazawa wapewa kipaumbele

📌Wakandarasi watakiwa kufanya kazi kwa weledi, ubora na kasi

📌Watakiwa kuepukana na vitendo vya rushwa

📌Wahimizwa kufuata Sheria, Kanuni na Taratibu za Nchi


Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) imesaini mikataba 30 yenye thamani ya shilingi Trilioni 1.2 kwa ajili ya kutekeleza Mradi wa Kusambaza Umeme katika Vitongoji 9,009 utakaonufaisha Wateja wa awali 290,300  katika mikoa 25 ya Tanzania Bara.

Akizungumza katika hafla hiyo leo, Januari 17, 2026 Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi amesema kusaini kwa mikataba ya Mradi huo ni utekelezaji wa maelekezo ya Serikali ya Awamu ya Sita, inayoongozwa na Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha ifikapo 2030 vitongoji vyote nchini viwe vimefikishiwa nishati ya umeme.

“Serikali imedhamiria kuhakikisha hakuna Mtanzania atakayebaki bila umeme. Tumekamilisha vijijini na sasa ni zamu ya vitongoji na kwa mikataba hii iliyosainiwa hivi leo ni ushahidi wa dhamira hiyo ya Serikali,” amesema Mhe. Ndejembi.

Amebainisha kuwa kati ya mikataba 30 iliyosainiwa, mikataba 21 ni ya kampuni za Wazawa na mikataba mingine tisa ni ya kampuni kutoka Nje ya nchi ambazo zimesajiliwa hapa nchini.

Serikali ya Rais Samia inatambua Sekta ya Nishati ni injini ya kuchochea maendeleo na amekuwa akitoa fedha nyingi ili kuboresha maisha ya Wananchi wa vijijini.

Ameipongeza REA kwa kuendelea kuwa chombo imara cha Serikali kwa utekelezaji wa Miradi mbalimbali ya kusimamia na kupeleka nishati bora kwa Wananchi na ameendelea kuhakikisha kuwa Taasisi zote za Umma ziunganishwe na umeme zikiwemo shule za msingi, sekondari na vituo vya afya.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amesema Serikali itaendelea na kasi yake ya kusambaza umeme ili kuleta tija inayokusudiwa.

Naye, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mhe. Subira Mgalu amepongeza jitihada za REA katika kutimiza azma ya Serikali ya kuhakikisha nishati ya umeme inasambaa kote nchini.

"Hongereni REA mnafanya kazi kubwa, leo hii tumefurahi kushuhudia tukio la kihistoria la kusaini mikataba ya kusambaza umeme vitongojini," amepongeza.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Meja Jenerali Mstaafu, Mhe. Balozi Jacob Kingu aliwasisitiza Wakandarasi kuzingatia thamani ya fedha za umma zilizotolewa kutekeleza Miradi sambamba kujifunza kutoka kwenye Miradi iliyokamilika ili kutekeleza kwa ufanisi na kwa ubora unaotakiwa.

Akizungumzia utekelezaji wa Miradi mbalimbali, Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mha. Hassan Saidy amesema REA inatekeleza azma ya Serikali ya kuhakikisha umeme unawafikia Wananchi kwa vitendo.

"Hadi kufikia mwishoni mwa mwaka 2025, Serikali imefanikiwa kufikisha umeme katika vijiji vyote 12,318 vya Tanzania Bara. Hatua hii imeleta mapinduzi ya kweli ya kiuchumi na kijamii, ikichangia kuboresha maisha ya Wananchi wanaoishi vijijini," amefafanua.

Amesema mwaka 2021 kati ya vitongoji 64,359 vilivyopo Tanzania Bara, vitongoji 28,258 pekee vilikuwa na umeme wakati vitongoji 36,101 vilikosa huduma hiyo muhimu.

Amefafanua kuwa kupitia utekelezaji wa Miradi mbalimbali kuanzia mwaka 2021 hadi Desemba 2025, Serikali imeunganisha umeme katika vitongoji 10,745, na hivyo kuongeza idadi ya vitongoji vyenye umeme kufikia 39,003.

Aidha, amesema vitongoji 2,435 vipo katika hatua za utekelezaji wa miradi inayoendelea na hivyo kufanya jumla ya vitongoji 41,438 kuwa tayari vimeunganishwa au vipo katika utekelezaji.

"Utekelezaji wa miradi hii ni utekelezaji wa maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha vitongoji vyote vinasambaziwa umeme," amefafanua.

Amesema Mradi utatekelezwa kwa kipindi cha miaka mitatu na aliwasisitiza Wakandarasi kuhakikisha wanafanya kazi kwa weledi na kujiepusha na vitendo vya rushwa na tabia zisizo na maadili.

"Mradi huu utahusisha ujenzi wa kilomita 13,180 za njia za msongo wa kilovolti 33, kilomita 14,016 za njia za msongo wa volti 415,

pamoja na ujenzi wa mashineumba 9,009 na utatekelezwa kupitia mafungu 30 ambapo mafungu 21 yakitekelezwa na kampuni za ndani, na mafungu 9 na kampuni za nje zilizosajiliwa nchini," amefafanua.

Amebainisha kwamba kwa kuzingatia gharama na idadi ya vitongoji vitakavyofikiwa, Mradi huo, ndiyo mkubwa zaidi kwa usambazaji umeme kuwahi kutekelezwa nchini.











Top News