Waziri Mavunde Afafanua Leseni za Utafiti Ndizo zinaibua Migodi Mikubwa, Kati

📍 Dodoma

Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, amesema Serikali inaendelea na Marekebisho ya Mfumo wa Kidigitali wa  Leseni za Utafiti wa Madini utakaosimamia hatua zote za utoaji na usimamizi wa leseni hizo.

Amesema mfumo huo utahusisha utoaji wa leseni, uwasilishaji wa taarifa za kila robo mwaka, utoaji wa hati za makosa, na hata kufutwa kwa leseni pale inapobidi bila kuhitaji uingiliaji wa moja kwa moja wa binadamu.

“Baada ya mfumo huu kukamilika, hamtaniona tena natangaza kufuta leseni. Leseni itajiondoa yenyewe kupitia mfumo huu. Mfumo utakuletea taarifa zote muhimu, utakukumbusha muda wa kuwasilisha taarifa, utatoa hati za makosa pale inapobidi, na hatimaye utafuta leseni wenyewe moja kwa moja endapo masharti hayatatekelezwa,” amesisitiza Waziri Mavunde.

Mhe. Mavunde ameyasema hayo Aprili 16, 2026, alipokuwa akizungumza katika kipindi cha Morning Trumpet kinachorushwa na runinga ya UTV. Ameongeza kuwa leseni za utafiti ni msingi muhimu wa kuibua migodi mikubwa na ya kati, na kwamba maeneo yanayoshikiliwa bila kuendelezwa yanaikosesha Serikali mapato, ajira, pamoja na fursa katika mnyororo mzima wa thamani wa Sekta ya Madini.

Ameeleza hayo kufuatia uamuzi wake wa Aprili 15, 2026, wa kuielekeza Tume ya Madini kufuta leseni 40 za utafiti wa madini zenye jumla ya eneo la kilomita za mraba 900 (sawa na hekari 188,163), baada ya wamiliki wake kushindwa kutekeleza masharti ya leseni licha ya kupewa hati za makosa.

Aidha, Waziri Mavunde amesema Serikali imejipanga kuimarisha usimamizi wa Sheria ya Madini kwa kuondoa tabia ya mazoea iliyokuwepo kwa muda mrefu, akisisitiza kuwa sekta hiyo inahitaji wawekezaji wenye dhamira ya dhati ya kuendeleza rasilimali za madini kwa manufaa ya taifa.

“Sekta ya Madini kuchangia asilimia 10.1 kwenye pato la taifa si jambo dogo. Tanzania tumepiga hatua kubwa. Fikiria kama tafiti kwenye leseni hizi zingekamilika tungekuwa na migodi mingapi mikubwa na ya kati?” amehoji.

Katika hatua nyingine, ametoa wito kwa vijana wanaopenda kuingia katika sekta ya madini kujiunga na kuanzisha vikundi rasmi ili waweze kufikiwa kwa urahisi na Serikali kupitia programu maalum ya Mining For A Brighter Tomorrow, inayolenga kuwawezesha vijana, wanawake na watu wenye ulemavu kupata leseni, mitaji na vifaa vya uchimbaji.

#MadininiMaisha&Utajiri

#Mining4Development

GEITA VIJIJINI: ZAIDI ya wananchi 700,000 kutoka kata 19 katika Mkoa wa Geita wanatarijiwa kunufaika na mradi mkubwa wa maji unaogharimu zaidi ya Sh bilioni 124 katika utekelezaji wake.

Mradi huo unatarajiwa kuanza kufanya kazi Septemba 30 mwaka huu na kuzalisha jumla ya lita milioni 45 za maji kwa siku.

Hayo yalibainishwa leo Aprili 16,2026 na Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira (GEUWASA), Mhandisi Frank Changawa mbele ya Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Kenani Kihongosi alipokagua utekelezaji wa mradi huo uliopo katika Kata ya Senga Geita Vijijini mkoani Geita.

Akizungumza baada ya kukagua mradi huo Kihongosi amesema huo ni miongoni mwa miradi ya miji 28 ambayo inatekelezwa nchi nzima na unatarajiwa kuleta mabadiliko makubwa ya kiuchumi na kijamii kwa upatikanaji wa maji safi na salama kwa ufanisi na kwa muda mrefu.

Amesema katika ilani ya Uchaguzi iliyopita, serikali iliahidi kuhakikisha huduma ya maji mijini inafikia asilimia 95 na vijijini asilimia 85, lakini mradi huo utakapokamilika, watavuka lengo hilo na kufikia upatikanaji wa maji kwa asilimia 100.

“Kwa kweli nikawa naona maajabu mengi, tumekagua miradi mingi, lakini huu ni mmoja wa miradi mikubwa sana. Hongereni sana, niwapongeze viongozi, wataalamu na wasimamizi wa mradi kwa weledi wao, mmeonesha umiliki mkubwa wa kitaaluma na kuhakikisha kazi inafanyika kwa ufanisi,” amesema Kihongosi.

Awali, akisoma taarifa ya mradi huo Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira (GEUWASA), Mhandisi Frank Changawa amesema gharama ya mradi huo ni dola milioni 53.463, na hadi sasa utekelezaji umefikia asilimia 80 ya kazi nzima ya ujenzi na miundombinu.




Farida Mangube, Morogoro

Serikali kupitia Mfuko wa Misitu Tanzania (TaFF) imeendelea kuimarisha uhifadhi wa misitu na maendeleo ya jamii kwa kutoa ruzuku zinazolenga kukuza miradi endelevu ya mazingira na uchumi wa kijani.

Hayo yamebainishwa katika ufunguzi wa mafunzo kwa wanufaika wapya wa ruzuku kwa mwaka wa fedha 2025/2026 yaliyofanyika Morogoro, yakikutanisha wanufaika, waratibu wa miradi, maafisa misitu pamoja na maafisa nyuki kutoka mikoa yote nchini.

Akizungumza katika ufunguzi wa mafunzo hayo, Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu wa TaFF, Dkt. Tuli Salum Msuya, alisema mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo wanufaika katika kusimamia na kutekeleza miradi yao kwa ufanisi, hususan katika usimamizi wa fedha za ruzuku, utekelezaji wa mikataba pamoja na uandaaji wa taarifa za maendeleo ya miradi.

Alisema Serikali chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuweka kipaumbele katika sekta ya misitu kama mhimili muhimu wa uhifadhi wa mazingira, kuongeza uzalishaji na kukuza sekta ya utalii kupitia misitu endelevu.

Kwa mwaka wa fedha 2025/2026, jumla ya miradi 137 imeidhinishwa kupatiwa ruzuku kati ya zaidi ya maombi 400 yaliyowasilishwa, ambapo miradi hiyo inatekelezwa katika wilaya zaidi ya 40 nchini.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Miradi na Mipango TaFF, Johnny Richard Mbwambo, alisema mpaka sasa TaFF imetoa shilingi bilioni 70 kuwezesha miradi ya misitu na ufugaji nyuki, hatua iliyochangia upandaji miti katika mashamba zaidi ya 290 pamoja na kuimarisha uhifadhi wa maeneo makubwa ya misitu nchini.

Mbwambo aliongeza kuwa awali baadhi ya changamoto zilijitokeza katika matumizi ya fedha na utoaji wa taarifa, hali iliyosababisha kuanzishwa kwa mafunzo kabla ya utekelezaji wa miradi ili kuongeza uwajibikaji na ufanisi.

Kwa upande wao, wanufaika wa ruzuku hiyo walisema mafunzo hayo yamewasaidia kupata uelewa mpana kuhusu usimamizi wa miradi na matumizi sahihi ya fedha za ruzuku, huku wakisisitiza umuhimu wa kufanya kazi kwa ushirikiano na kuhakikisha fedha zinatumika kwa malengo yaliyokusudiwa.

Kwa sasa, takriban vikundi 79 vinanufaika na miradi inayofadhiliwa na TaFF, ikiwemo shughuli za kilimo na ufugaji nyuki zinazochangia uhifadhi wa misitu ya asili. 







Na Mwamvua Mwinyi, Pwani, April 16, 2026
MKOA wa Pwani umejipanga kupokea Mwenge wa Uhuru Aprili 18, 2026, huku wananchi wakihimizwa kujitokeza kwa wingi katika Shule ya Msingi Mtambani, Kata ya Mapinga, wilayani Bagamoyo, ambapo mwenge huo utapokelewa ukitokea Kinondoni, jijini Dar es Salaam.

Mkuu wa Mkoa huo Abubakar Kunenge, akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake kuhusu ujio wa Mwenge wa Uhuru, alieleza mwenge utakagua, kuzindua na kuweka mawe ya msingi katika miradi mbalimbali ndani ya halmashauri tisa zilizopo katika wilaya saba.

“Sisi tumejipanga kama tulivyofanya vizuri mwaka uliopita, na mwaka huu kama kawaida yetu tumeweka miradi inayogusa maslahi ya wananchi. Haturudii miradi, na tunamshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutupatia fedha za kutosha kwa ajili ya miradi ya maendeleo,” alifafanua Kunenge.

Aliongeza kuwa mwaka uliopita mkoa huo ulipata jukumu la kuwasha Mwenge wa Uhuru kitaifa na ulifanya vizuri kwa kushika nafasi ya kwanza.

Aidha, katika tathmini ya halmashauri 184 za Tanzania Bara na Zanzibar, Chalinze ilishika nafasi ya pili, Manispaa ya Kibaha nafasi ya tatu, Bagamoyo nafasi ya tisa na Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha nafasi ya 11.

Kunenge alibainisha kuwa,lengo la Mbio za Mwenge wa Uhuru ni kuimarisha umoja, mshikamano na udugu miongoni mwa Watanzania.

Alieleza baada ya kupokelewa, Aprili 18 utapokelewa na kukimbizwa halmashauri ya Bagamoyo, Aprili 19 Chalinze, Aprili 20 Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha, Aprili 21 Manispaa ya Kibaha, Aprili 22 Mafia, Aprili 23 Kisarawe, Aprili 24 Mkuranga, Aprili 25 Kibiti, Aprili 26 Rufiji na Aprili 27 utakabidhiwa mkoani Lindi.

Kwa mwaka 2026, Mwenge wa Uhuru umebeba ujumbe wa kudumisha amani, umoja na mshikamano wa kitaifa chini ya kauli mbiu isemayo: “Tanzania ni Yetu Sote, Tushikamane kwa Pamoja Kuleta Maendeleo.”

Vilevile mbio hizo pia hubeba jumbe za kudumu zikiwemo kuimarisha mapambano dhidi ya VVU/UKIMWI, dawa za kulevya, lishe bora na vita dhidi ya rushwa.

Kutokana na umuhimu huo, aliwataka wananchi kujitokeza kwa wingi kushiriki katika shughuli za Mwenge wa Uhuru katika wilaya zote utakazopitia.

Na Mwandishi wetu
WIZARA ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imeanza kuweka utaratibu wa kutumia hazina ya maarifa na uzoefu kutoka kwa Mabalozi Wastaafu ili kuimarisha utekelezaji wa mipango mbalimbali ya kuimarisha diplomasia ya nchi.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo , amebainisha utaratibu huo leo Aprili 15, 2026, jijini Dar es Salaam wakati anafungua kikao cha mashauriano kati ya uongozi wa Wizara na Mabalozi Wastafu.

"Wizara tumeanzisha utaratibu wa kuwa na vikao vya mara kwa mara na Mabalozi Wastaafu ili kuvuna maarifa na uzoefu wao kwa lengo la kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia ili ulete nanufaa katika nyanja mbalimbali kama vile, siasa, ulinzi na usalama, uchumi, biashara, uwekezaji na utalii". Balozi Kombo alisema

Balozi Kombo ametaja mifano ya maeneo ambayo angependa Mabalozi Wastaafu wachangie maarifa na uzoefu walio kuwa nao ili maeneo hayo yaendelee kuwa na manufaa zaidi kwenye nchi.

Maeneo hayo ni pamoja na mwenendo wa ufanyaji wa biashara baina ya Tanzania na nchi nyingine, hususan zilizopo barani Afrika.

Amesema utekelezaji wa Dira 2050 ambayo inalenga uchumi wa dola bilioni moja, ni eneo lingine muhimu ambalo maarifa ya Mabalozi Wastaafu yanahitajika ili kuhakikisha utekelezaji wake unakuwa wa ufanisi.

Waziri Kombo ameongeza kuwa mabadiliko yanayoendelea duniani hususan, maendeleo ya kidigitali yanahitaji mikakati thabiti ili nchi iweze kunufaika na kuwa na mipango madhubuti ya kukabiliana na athari zake. Haya yote yanahitaji mawazo ya pamoja ili kuyaendeea kwa ufanisi.

Eneo lingine ambalo Waziri Kombo alisisitiza umuhimu wa kupata uzoefu wa Mabalozi Wastaafu ni siasa za ulimwengu ambazo zimekuwa hazitabiriki na zinasababisha madhara mbalimbali, hususan katika nchi zinazoendelea kama Tanzania.

Aidha, uzoefu wa Mabalozi Wastaafu unahitajika katika kuendeleza na kuimarisha taswira nzuri ya nchi na hasa nchi inapopewa dhamana ya majukumu ya kimataifa. Balozi Kombo alisema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika mwaka 2028 na hivyo maarifa yao ni muhimu ili kuhakikisha nchi inatekeleza jukumu hilo kwa ufanisi.

Awali, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo alisema Wizara inaangalia uwezekano wa kuanzisha utaratibu rasmi kupitia Ofisi ya Rais-UTUMISHI ili ushirikishwaji wa Mabalozi Wastaafu uwe unatambulika rasmi.
Na Khadija Kalili
BARAZA la Madiwani la Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha limepitisha bajeti ya Mil. 50 kwa kila Kata zitakazotumika kwa ajili ya kufungua barabara zillizoharibika na kukarabati miundombinu ya barabara zilizoharibiwa na mvua zinazoendelea kunyesha.

Fedha hizo zimepitishwa kufuatia kikao cha kikanuni na Baraza hilo lililofanyika tarehe 14, 2026 ambapo utekelezaji wake ni katika kipindi cha mwaka wa fedha 2026-2027.

Mstahiki Meya wa Manispaa ya Kibaha Dkt. Mawazo Nicas amesema kuwa awali fedha hizo zilitengwa kiasi cha Mil.30 kwa kila Kata lakini kutokana na kubaini ubovu wa barabara hizo wamelazimika kuongeza bajeti hiyo hadi kufikia Mi.50.

"Tunatambua kwamba Manispaa ya Kibaha kuna Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini (TARURA) Pamoja na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS )

lakini Manispaa tumeona ni vema kutoa fedha hizo na kuzifungua baadhi ya barabara kwa dharula ili kupunguza changamoto ya ubovu wa barabara.

Mstahiki Meya Dkt.Nicas amezitaja Kata 14 zitakazopata Mi.50 kuwa ni Mailimoja, Tumbi,Pangani, Picha ya Ndege,Kongowe, Mkuza na Tangini.

Kata zingine ni Viziwaziwa, Msangani, Kibaha,Mbwawa,Visiga,Misugusugu na Tumbi.
Dkt.Nicas amewapongeza madiwani wa Manispaa hiyo kwa kuridhia bajeti hiyo inayokwenda kutatua kero ya barabara kadhalika amempongeza Mkurugenzi wa Manispaa ya Kibaha Dkt.Rogers Shemwelekwa kwa kazi nzuri ya kukusanya mapato ambayo yanasaidia kutatua kero za wananchi.

"Wananchi wetu kilio chao kikubwa ni miundombinu barabara hizi zipo chini ya TARURA na TANROADS lakini kwa upendo wa Wataalamu na Madiwani kuwajali wananchi wake wameamua kutenga fedha hizo ambazo ni mapato ya ndani zikatumike kurekebisha maeneo korofi", amesema.

Diwani wa Kata ya Sofu Mashaka Mahande amesema kutengwa kwa fedha hizo kunakwenda kupunguza kero ya barabara ambazo nyingi zimeharibika zaidi kipindi cha mvua.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na wadau wa Sekta ya Afya pamoja na wageni mbalimbali kabla ya kufungua Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na wadau wa Sekta ya Afya pamoja na wageni mbalimbali kabla ya kufungua Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Tuzo ya Heshima ya Kibinadamu ya Upasuaji wa Ubongo kutoka kwa Rais wa Chama cha Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu Tanzania (TNS) Dkt. Othman Kiloloma kwenye hafla ya ufunguzi wa Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Tuzo ya Heshima ya Kibinadamu ya Upasuaji wa Ubongo kutoka kwa Rais wa Chama cha Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu Tanzania (TNS) Dkt. Othman Kiloloma kwenye hafla ya ufunguzi wa Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.
Wafanyakazi wa Sekta ya Afya wakiwa kwenye hafla ya ufunguzi wa Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.
Wadau wa Sekta ya Afya wakiwa kwenye hafla ya ufunguzi wa Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.


Na Said Mwishehe, Michuzi TV


MWENYEKITI wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) Deodatus Balile, amesema matukio ya waandishi wa habari kukamatwa, kupigwa na kubughudhiwa yamepungua kwa kiasi kikubwa ukilinganisha na hali ilivyokuwa huko nyuma.

Balile amesema hayo leo Aprili 16, 2026 wilayani Temeke mkoani Dar es Salaam katika ufunguzi wa Mkutano Mkuu Maalumu wa jukwaa hilo uliofanyika kwa lengo la kujadili mapendekezo ya marekebisho ya Katiba.

Akizungumzia hali ya vyombo vya habari nchini na mataifa mengine, Balile amesema kumetokea mambo mengi yakiwemo waandishi kupoteza maisha, vyombo vya habari kufungwa na kukabiliwa na hali ngumu ya kiuchumi.

“Mataifa mbalimbali duniani tumeshuhudia mambo mengi yakitokea katika miaka ya karibuni kwenye tasnia yetu ya habari.

“Waandishi 140 wamepoteza maisha kutokana na vita zinazoendelea kwa baadhi ya nchini, lakini tumeshuhudia katika vyombo vya wenzetu wamepata mtanzuko mkubwa na sasa hivi Sauti ya Amerika (VOA) haipo hewani na chaneli zake zote.

“Pia katika nchi za jirani kuna waaandishi wamezuiliwa kuingia katika nchi. Kwa Tanzania matukio ya waandishi wa habari kukamatwa, kupigwa imepungua kwa kiasi kikubwa ukilinganisha na zamani.

“Nimekuwa Rais wa Jukwaa la Wahariri la Afrika Mashariki kwa muda mrefu, na nchi ambazo ni wanachama wa jukwaa hilo wanakiri Tanzania iko vizuri, lakini ni wajibu wetu sasa kuzingatia misingi ya taaluma ya habari," amesema.

Akieleza zaidi Balile amesema kuna baadhi ya waandishi wa habari wamekuwa wakiogopa kuandika kabla ya kuzuiliwa kwa maana ya kujizuia kuandika kabla ya kuzuiwa, hivyo ametoa rai ya kuondoa woga huo huku akisisitiza kutekeleza majukumu yao kwa kufuata misingi ya taaluma.


UCHUMI WA VYOMBO VYA HABARI

Kuhusu hali ya uchumi katika vyombo vya habari amesema umekumbwa na changamoto kubwa katika mataifa mbalimbali akitolea mfano nchini Marekani ambako magazeti 3,200 yamefungwa na kuondoka sokoni.

Pia, magazeti yaliyokuwa yakipata faida ya mamilioni ya fedha sasa yanajiendesha kwa faida ndogo akitolea mfano kampuni ya Standard nchini Kenya.

“Kwa Tanzania kampuni kama New Habari iliweka historia kwa kujiondoa yenyewe sokoni. Takwimu sio nzuri sana kwa kuwa mapato yamepungua sio katika vyombo vya habari pekee, lakini hadi katika taasisi za habari na sisi Jukwaa la Habari tumekuwa na changamoto za kiuchumi na ndio maana hatujakutana kwa muda mrefu,” amesema.

Kutokana na hali hiyo ametoa rai kwa vyombo vya habari nchini kutafuta vyanzo vipya vya mapato badala ya kutegemea vilivyopo hasusan matangazo na mabaki ya magazeti.

Pamoja na hayo, kwa kipekee ametoa shukrani za dhati kwa niaba ya jukwaa hilo kwa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) kutokana na kuendelea kuliunga mkono jukwaa la Wahariri.

“Kwa kipekee tunaishukuru WCF kwa kuendelea kutuamini siku hadi siku na wamekuwa wakituwezesha kwa kiwango kikubwa kwa mfano kama walianza kutuchangia kwa sh. milioni tano wakaongeza milioni 10, milioni 15, hadi Sh. milioni 30. Kwa hiyo kwa kipekee tunaishukuru WCF kwa kuendelea kuwa nasi wakati wote.” amesisitiza.





Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa - Mambo ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa (SUKI), Ndg. Rabia Abdalla Hamid, amefanya Kikao kazi na Kansela wa Chama Cha Kikomunisti (CPC), Ubalozi wa China nchini Tanzania Ndg. Xu Sujiang leo tarehe 16.04.2026, Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Lumumba, Dar es Salaam.

Lengo la kikao hicho ni kujadiliana kuhusu masuala mbalimbali yanayolenga kuimarisha uhusiano na itikadi za vyama hivyo.










Na Mwandishi wetu

Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola ambaye pia ni Rais wa zamani wa Malawi, Mhe. Lazarus McCarthy Chakwera ameondoka nchini Aprili 16, 2026, kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) na kuagwa na viongozi waandamizi wa serikali wakiongozwa na Balozi wa Tanzania nchini Uingereza, Mhe. Mberwa Kairuki, baada ya kumaliza ziara yake ya kikazi ya siku 9 nchini Tanzania.

Mhe. Chakwera ambaye aliwasili nchini Aprili 8, 2026 kwa ziara ya kikazi, alikutana na kufanya mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Mawaziri akiwemo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo pamoja na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - Sera, Bunge, Uratibu Wenye Ulemavu, Prof. Palamagamba Kabudi ambaye aliongoza ujumbe wa Serikali kukutana na Mjumbe huyo Maalum.

Katika kikao na ujumbe wa Serikali, Mhe. Profesa Kabudi alimueleza kwa kina Mhe. Chakwera, kuhusu hatua mbalimbali zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuimarisha demokrasia nchini huku ikiweka msisitizo katika kulinda na kuheshimu utu wa Mtanzania, kuzingatia haki na uwajibikaji, amani na utulivu pamoja na kudumisha umoja wa kitaifa.

Kikao hicho na Mjumbe huyo Maalum kilikuwa chenye mafanikio baada ya Mhe. Chakwera kuelezwa namna serikali inavyoendelea kuchukua hatua mbalimbali hususani katika kudumisha amani, umoja wa kitaifa na ustawi wa Watanzania na kuhakikisha nchi inaendelea kuwa tulivu na kumuwezesha kila Mtanzania kushiriki kikamilifu katika kujenga uchumi jumuishi na kujiletea maendeleo.

Mbali na kukutana na ujumbe wa Serikali, Mheshimiwa Chakwera alifanya mazungumzo na Msajili wa Vyama vya Siasa, Mhe. Jaji Mstaafu Francis Mutungi, na pia vyama vya siasa vya ACT–Wazalendo, Chama cha National League for Democracy (NLD), United Democratic Party (UDP), Chama cha National Reconstruction Alliance (NRA), Chama cha NCCR Mageuzi, Chama cha Sauti ya Umma (SAU), Chama cha Alliance for Democratic Change (ADC), Alliance for African Farmers Party (AAFP) na Chama cha ADA-TADEA.

Vyama vingine ni pamoja na Democratic Party (DP), Tanzania Labour Party (TLP), Union for Multiparty Democracy (UMD), United People’s Democratic Party (UPDP), Chama cha Kijamii (CCK), Demokrasia Makini, Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMA) na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).

Mjumbe huyo Maalum pia alikutana na wadau mbalimbali akiwemo Mwenyekiti wa Tume ya Uchunguzi wa matukio yaliyotokea Oktoba 29, 2025 na baada ya Uchaguzi Mkuu, Jaji Mkuu Mstaafu Mhe. Mohamed Othman Chande, Waziri Mkuu Mstaafu na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jaji Joseph Warioba, Jumuiya zisizo za Kiserikali, Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar, Mhe. Jaji George Joseph Kazi, Mwenyekiti wa ACT – Wazalendo Mhe. Othman Masoud Othman, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Mussa Azzan Zungu, Jaji Mkuu wa Mahakama ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Jaji George Mcheche Masaju, Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele na Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi Mhe. Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro.

Akiwa nchini, Mhe. Chakwera alipata fursa ya kujionea namna Tanzania ilivyowekeza katika sekta ya usafiri ambapo wakati akienda Zanzibar kukutana na viongozi wa kisiasa kisiwani humo, alitumia usafiri boti ya kisasa inayofanya safari zake katika ya Dar es Salaam na Unguja, wakati akielekea Dodoma alitumia usafiri wa treni ya mwendokasi (SGR) na kufurahia namna Serikali ilivyowekeza na kuimarisha sekta ya usafiri nchini.

Ziara ya Mhe. Chakwera imekuwa ya mafanikio na kuionesha Afrika na dunia hali ya Amani na utulivuza iliyopo nchini Tanzania, licha ya changamoto zilizojitokeza wakati na baada ya uchaguzi mkuu, na namna ambavyo Serikali imeendelea kuchukua hatua madhubuti za kushughulikia changamoto hizo huku ikisimamia misingi ya kuimarisha demokrasia, Amani, utulivu na kuhakikisha kila mtanzania anashiriki vema katika kujenga uchumi na kuifikia Dira 2050 ambapo ifikapo mwaka 2050, Tanzania inalenga kuwa na uchumi wa dola za Marekani trilioni 1, huku kipato cha mtu mmoja mmoja kikizidi dola za Marekani 7,000.

Katika ziara yake hiyo, Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola aliwezeshwa kukutana na wadau wote aliohitaji kukutana nao pamoja na wale wote walioainishwa na Sekretarieti ya Jumuiya ya Madola.














Top News