Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa amesimama wakati akipokea heshima ya wimbo wa Taifa mara baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Vnukovo, Jijini Moscow kwa ajili ya Ziara ya Kitaifa nchini Urusi tarehe 02 Juni, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Vnukovo, uliopo Jijini Moscow kwa ajili ya Ziara ya Kitaifa, nchini Urusi tarehe 02 Juni, 2026. Ziara hii ina lenga kuimarisha uhusiano wa Kidiplomasia, kisiasa, kiuchumi na kihistoria baina ya Tanzania na Urusi.

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Vnukovo, uliopo Jijini Moscow kwa ajili ya Ziara ya Kitaifa, nchini Urusi tarehe 02 Juni, 2026. Ziara hii ina lenga kuimarisha uhusiano wa Kidiplomasia, kisiasa, kiuchumi na kihistoria baina ya Tanzania na Urusi.

Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Kenani Kihongosi, amewataka wananchi wa Wilaya ya Babati mkoani Manyara kuwa makini wanapowapokea wageni katika maeneo yao ili kuepuka madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na kuwapokea watu wasiowafahamu vizuri.

Kihongosi ametoa wito huo leo Juni 2,2026 aliposhiriki kikao cha Shina namba Mbili Kata ya Bonga wilayani Babati mkoani Manyara.

Akizungumza mara baada ya kusikiliza ajenda ya kikao hicho Kihongosi amesema pamoja na kwamba Watanzania wana sifa ya ukarimu na upendo kwa wageni, ni muhimu kuhakikisha wageni wanaopokelewa wanajulikana na hawana nia ya kuleta matatizo katika jamii.

“Nimeelezwa kwamba mnawapokea wageni wanaofika katika maeneo yenu na kuwachukulia kama ndugu. Hilo ni jambo jema na linaonyesha ukarimu na mshikamano uliopo katika jamii yetu,” amesema Kihongosi.

Ameongeza kuwa ukarimu huo unapaswa kuambatana na tahadhari ili kulinda usalama wa wananchi na maeneo yao.

“Hata hivyo, mnapopokea wageni ni muhimu kuchukua tahadhari na kujiridhisha kuwa ni watu salama. Tusije tukawapokea watu wenye nia mbaya au wahalifu ambao wanaweza kuleta matatizo katika maeneo yetu,” amesema.

Kihongosi amesisitiza kuwa viongozi wa maeneo na wananchi wanapaswa kushirikiana kuhakikisha taarifa za wageni wanaoingia katika jamii zinajulikana ili kuimarisha ulinzi na usalama.

“Ni wajibu wa viongozi na wananchi kuhakikisha taarifa za wageni wanaoingia katika maeneo yao zinajulikana na, inapobidi, zinawasilishwa kwa vyombo husika vya usalama. Hii itasaidia kulinda amani, usalama na utulivu wa maeneo yetu,” amesema.

Ameongeza kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kuzuia uwezekano wa watu wenye nia ovu kujificha ndani ya jamii na kusababisha changamoto za kiusalama.

Katika hatua nyingine, Kihongosi amewataka wananchi kuendelea kulinda amani na mshikamano uliopo nchini, akisema Tanzania imeendelea kuwa mfano wa utulivu kutokana na umoja na upendo wa wananchi wake.

“Tanzania yetu haigawanyiki Mungu alivyotupa nchi hii, na kama ambavyo nyinyi watu wa Babati mmepewa ardhi hii kuwa makazi yenu, basi mna wajibu wa kuilinda. Hapa ni nyumbani kwenu, msikubali mtu yeyote aje kucheza na utulivu wa maeneo yenu,” amesema.













-Masoko ya Kaboni Kufungua Fursa Mpya za Ajira na Uwekezaji


Na Chalila Kibuda,Michuzi TV

Kituo cha Taifa cha Kuratibu Kaboni (NCMC) kimesema kuwa mustakabali wa ajenda ya mabadiliko ya tabianchi na uchumi wa kijani nchini unategemea nguvu, ubunifu na uongozi wa vijana, huku kikihimiza ushiriki wao katika kutumia fursa zinazotokana na sekta hiyo inayokua kwa kasi duniani.

Akizungumza katika Mkutano wa Vijana wa mwaka 2026 uliofanyika jijini Dar es Salaam, Afisa Mtendaji Mkuu wa NCMC, Kathryn Kigaraba, amesema mabadiliko ya tabianchi yameendelea kuwa moja ya changamoto kubwa zinazoikabili dunia, lakini pia ni miongoni mwa fursa muhimu za kiuchumi zinazoweza kuleta maendeleo makubwa kwa Tanzania.

Kathryn amesema tayari Tanzania inaendelea kushuhudia athari za mabadiliko ya tabianchi kupitia mabadiliko ya mifumo ya mvua, ukame, mafuriko, uharibifu wa mifumo ikolojia pamoja na changamoto mbalimbali zinazoathiri maisha ya wananchi.

Amesema hali hiyo inahitaji hatua za haraka na ushiriki wa makundi yote ya jamii, hususan vijana.

Aidha, amesema dunia inaelekea katika uchumi wenye matumizi madogo ya kaboni na unaostahimili athari za Mabadiliko ya tabianchi, jambo ambalo tayari limeanza kuzalisha mamilioni ya ajira na kuvutia uwekezaji wa mabilioni ya dola katika sekta za nishati jadidifu, kilimo himilivu, teknolojia za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, urejeshaji wa misitu, masoko ya kaboni, fedha za Mabadiliko ya tabianchi pamoja na usimamizi wa taka.

Kathryn amesema Tanzania ina nafasi kubwa ya kunufaika kutokana na fursa hizo kwa kuwa na rasilimali nyingi za asili zikiwemo misitu ya miombo, maeneo ya mikoko, maeneo ya kilimo na bioanuwai yenye uwezo mkubwa wa kuvutia uwekezaji katika miradi ya kaboni na hatua nyingine za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

“Vijana ndiyo kundi kubwa zaidi la wananchi nchini. Ni wabunifu, wajasiriamali, watafiti na viongozi wa baadaye wenye uwezo wa kuongoza mageuzi ya uchumi wa kijani. Hatupaswi kuwaona kama wanufaika pekee wa hatua za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, bali wawe viongozi wa mabadiliko hayo,” amesema.

Amesema NCMC inalenga kuona vijana wa Tanzania wakijitokeza kuwa wataalamu wa masoko ya kaboni, wabunifu wa nishati jadidifu, wataalamu wa fedha za Mabadiliko ya tabianchi, wataalamu wa mifumo ya taarifa za kijiografia (GIS), wataalamu wa ufuatiliaji wa mazingira kwa kutumia teknolojia za kisasa pamoja na wabunifu wa suluhisho za kidijitali za kufuatilia na kuripoti masuala ya mabadiliko ya tabianchi.

Aidha, amewataka vijana kuzingatia maeneo matatu muhimu ambayo ni ubunifu, ujasiriamali na uongozi ili waweze kunufaika kikamilifu na fursa za uchumi wa kijani.

Amesema ubunifu katika matumizi ya teknolojia za kidijitali, akili mnemba, mifumo ya ufuatiliaji wa mazingira na nishati safi utakuwa muhimu katika kutatua changamoto za mabadiliko ya tabianchi na kuijenga Tanzania ya baadaye yenye ustahimilivu.

Pia amesisitiza umuhimu wa vijana kuanzisha biashara katika maeneo ya upandaji miti, nishati safi za kupikia, urejelezaji wa taka, kilimo endelevu, huduma za mazingira pamoja na maendeleo ya miradi ya kaboni, akieleza kuwa uchumi wa kijani una uwezo mkubwa wa kuzalisha ajira na kuongeza kipato kwa wananchi.

Amesema kuna umuhimu kwa vijana kuwa mstari wa mbele katika kuhamasisha jamii, kushiriki katika utungaji wa sera na kulinda mazingira kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Amesema Serikali imeendelea kuimarisha utekelezaji wa mikakati ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kupitia Mkataba wa Paris, Michango ya Kitaifa ya Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi (NDCs), mifumo ya masoko ya kaboni pamoja na mipango mingine ya maendeleo endelevu.

Ameongeza kuwa NCMC itaendelea kusaidia juhudi hizo kupitia uhamasishaji wa uanzishaji wa miradi ya kaboni, mifumo ya ufuatiliaji, taarifa na uthibitishaji wa takwimu za kaboni (MRV), uhamasishaji wa fedha za Mabadiliko ya tabianchi, tafiti, ubunifu pamoja na kujenga uwezo kwa wadau mbalimbali.

Aidha, amesema vijana wanapaswa kujifunza ujuzi mpya na kutumia fursa zinazopatikana katika masoko ya kaboni, nishati jadidifu, kilimo endelevu na uhifadhi wa mazingira ili wawe sehemu ya kujenga Tanzania yenye ustahimilivu na maendeleo endelevu.

“Msisubiri mustakabali uje wenyewe. Uundeni, uongozeni na umilikini. Kwa pamoja tunaweza kubadili ajenda ya mabadiliko ya tabianchi kuwa chanzo cha fursa za uchumi wa kijani na kujenga Tanzania yenye ustawi kwa vizazi vya sasa na vijavyo,” amesema.


Afisa Mtendaji Mkuu wa NCMC, Kathryn Kigaraba akizungumza katika Mkutano wa Vijana wa mwaka 2026 uliofanyika jijini Dar es Salaam kuhusiana  mabadiliko ya tabianchi na fursa katika ya masoko ya Kaboni.
Na Chalila Kibuda,Michuzi TV

Vijana nchini wametajwa kuwa nguzo muhimu katika juhudi za uhifadhi wa mazingira na maendeleo ya sekta ya kaboni, huku Serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo wakihimizwa kuongeza fursa za ajira, mafunzo na ushiriki wao katika kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi.

Hayo yameelezwa na Naibu Mkurugenzi Mtendaji Taasisi ya Kaboni Afrika (ACA) Kaley Milao katika kongamano la vijana lililofanyika Dar es Salaam, ambapo alisema kuwa changamoto za tabianchi zinaweza kubadilishwa kuwa fursa za maendeleo, ubunifu na ajira kwa vijana wa Tanzania na Afrika kwa ujumla.

Amesema ACA imekuwa mstari wa mbele katika kuhamasisha ushiriki wa vijana kwenye masuala ya mazingira kupitia mikutano na programu mbalimbali zinazolenga kujenga uelewa na uwezo wa kizazi kipya katika sekta ya kaboni na uhifadhi wa mazingira.

Kaley mafanikio yaliyopatikana, alisema kupitia kongamano la Green Youth Summit 2025, wanafunzi watano kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam walipata ajira za muda mfupi huku mwanafunzi mmoja wa kike akipata ajira ya kudumu, hatua iliyolenga kuwawezesha vijana kitaaluma na kiuchumi.

Aidha amesema ACA imeendelea kutekeleza programu ya inayotumia michezo, elimu na ubunifu kuhamasisha watoto na vijana kuhusu umuhimu wa kulinda mazingira, kwa lengo la kujenga kizazi chenye uelewa wa masuala ya mazingira tangu utotoni.

Katika kongamano hilo, ACA ilitoa wito kwa taasisi mbalimbali ikiwemo Kituo cha Taifa cha Ufuatiliaji wa Kaboni (NCMC), Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) pamoja na Wizara ya Maliasili na Utalii kuongeza nafasi za ajira, mafunzo kwa vitendo na fursa nyingine kwa vijana ili kuimarisha uwezo wao wa kiuchumi na kitaaluma.

Mtendaji huyo alisema vijana wengi wana mawazo, ubunifu na nguvu kazi kubwa inayoweza kuchangia maendeleo ya taifa, lakini wanahitaji kuaminiwa, kupewa nafasi na kuwezeshwa kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo.

Aidha amesema ACA imeipongeza Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kwa juhudi zake katika kuimarisha agenda ya mazingira na mabadiliko ya tabianchi ndani na nje ya nchi.

Kongamano hilo limeelezwa kuwa sehemu ya juhudi za kujenga ushirikiano kati ya Serikali, taasisi za elimu, sekta binafsi na vijana katika kuhakikisha mazingira yanahifadhiwa huku yakitoa fursa za maendeleo endelevu kwa kizazi cha sasa na kijacho.
Naibu Mkurugenzi Mtendaji Taasisi ya Kaboni Afrika    (ACA) Kaley Milao  akizungumza katika kongamano la vijana lililofanyika Dar es Salaam kuhusiana na harakati ya Taasisi katika kuwainua vijana katika uhifadhi wa mazingira wa kupata kipato.

Utaratibu wa Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba wa kusikiliza na kutatua kero za wananchi kwa njia ya mazungumzo na maridhiano umewezesha kupatikana kwa suluhu ya mgogoro wa miaka 14 kati ya Bi. Martha Hilonga wa Mto wa Mbu mkoani Arusha na Parokia ya Mtakatifu Yuda Thadei ya Kanisa Katoliki Mto wa Mbu, Jimbo Kuu Katoliki la Arusha.

Mgogoro huo ulianza mwaka 2012 baada ya Bi. Martha Hilonga kupata ajali iliyohusisha gari la Parokia hiyo, hali iliyosababisha kupoteza mguu wake wa kulia. Tangu wakati huo, jitihada za kutafuta fidia kupitia vyombo mbalimbali ikiwemo Mahakama ziliendelea kwa miaka mingi bila kufikia suluhu ya kudumu.

Mwezi Februari 2026, wakati wa mkutano wa hadhara wa kusikiliza na kutatua kero za wananchi uliofanyika Mto wa Mbu wilayani Monduli, Bi. Martha aliwasilisha malalamiko yake kwa Waziri Mkuu akieleza kuwa licha ya kufuatilia haki yake kwa muda mrefu, bado hakuwa amepata fidia .

Baada ya kupokea malalamiko hayo, Waziri Mkuu alielekeza timu ya wataalamu kutoka Ofisi yake kwenda mkoani Arusha kwa lengo la kutafuta suluhu ya mgogoro huo kwa njia ya maridhiano. Timu hiyo ilifanya mazungumzo na Bi. Martha, viongozi wa Serikali, viongozi wa Kanisa Katoliki pamoja na wanasheria wa pande zote katika vikao vilivyofanyika kwa kipindi cha wiki mbili.

Mazungumzo hayo yalihitimishwa kwa makubaliano ya pande zote kuondoa shauri lililokuwa Mahakama ya Rufani na kumaliza mgogoro huo kwa njia ya maridhiano.

Katika maridhiano hayo, Jimbo Kuu Katoliki la Arusha lilikubali kumjengea Bi. Martha nyumba ya kuishi kutokana na athari za ulemavu wa kudumu alioupata kufuatia ajali hiyo.

Aidha, Waziri Mkuu ameahidi kumwezesha Bi. Martha kupata mtaji wa biashara utakaomsaidia kujitegemea kiuchumi. Kwa mujibu wa makubaliano yaliyosainiwa na pande zote, Kanisa Katoliki litajenga nyumba yenye vyumba viwili vya kulala, sebule, jiko na choo cha ndani katika kipindi kisichozidi miezi sita.

Akizungumza baada ya kufikiwa kwa maridhiano hayo, Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Arusha, Isaac Aman amesema Kanisa linaamini katika utu, upendo na mshikamano wa kijamii na kwamba litatekeleza makubaliano hayo kwa wakati ili kumaliza kabisa mgogoro huo.

Naye Bi. Martha Hilonga ameishukuru Serikali inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba kwa kusikiliza kilio chake na kufanikisha kupatikana kwa suluhu ya mgogoro uliodumu kwa miaka 14.

Kwa upande wake, Mwanasheria wa Jimbo Kuu Katoliki la Arusha, Bw. John Lawena amesema Kanisa litazingatia na kutekeleza kwa wakati masharti yote yaliyobainishwa katika nyaraka za maridhiano.

Maridhiano hayo yamehitimisha mgogoro uliodumu kwa zaidi ya muongo mmoja na kuwa mfano wa namna mazungumzo na ushirikiano kati ya wadau mbalimbali vinavyoweza kusaidia kutatua migogoro ya muda mrefu kwa amani na kuelewana.




Na Said Mwishehe,Michuzi TV

SIKU za karibuni Chama Cha Mapinduzi(CCM) kupitia Katibu Mkuu wake Dk.Asha-Rose Migiro kimevunja ukimya wa muda mrefu kwa kuamua kuzungumzia masuala mbalimbali tangu kutokea kwa vurugu Oktoba 29.

Kupitia mahojiano maalum yaliyofanywa na Mtangazaji wa Crown Media Salim Kikeke alitumia nafasi hiyo kuuliza maswali mbalimbali kwa CCM kupitia Katibu Mkuu Dk.Asha-Rose Migiro.

Kwa sehemu kubwa maswali ya Kikeke yalijikita katika ripoti ya Tume ya Kuchunguza matukio kabla na baada ya Oktoba 29 mwaka 2025.Tume hiyo ilikuwa ikiongozwa na Mwenyekiti Jaji Mstaafu Othman Chande.

Tunafahamu tangu kutolewa kwa ripoti hiyo ambayo ilikabidhiwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Samia Suluhu Hassan kumekuwepo na maswali mengi na kwa CCM tangu kutolewa kwa ripoti hiyo ilikuwa kimya.

Kwa majibu ya Katibu Mkuu wa CCM, Asha-Rose Migiro, inaonesha jambo moja muhimu ambalo viongozi wa chama hicho wameamua kulifanya baada ya kutolewa kwa ripoti ya Tume iliyoongozwa na Othman Chande; kwanza ni kutafakari kwa kina kabla ya kutoa msimamo rasmi wa kisiasa.

Kwa muda mrefu baada ya ripoti hiyo kutolewa, kulikuwa na maswali mengi kutoka kwa wananchi kuhusu ukimya wa CCM. Hata hivyo, katika majibu yake, Dk. Migiro ameonesha kuwa chama hakikutaka kutoa majibu ya haraka kutokana na uzito wa tukio lenyewe. 

Kauli yake kwamba viongozi wa CCM “waliduwaa” na “walishutuka” inaashiria kuwa chama kiliona matukio ya Oktoba 29 kama jambo lisilo la kawaida katika historia ya Tanzania. 

Hivyo, badala ya kujibu kwa haraka au kwa hisia, walichagua kuchukua muda wa kutafakari kilichotokea na athari zake kwa taifa.

Mtazamo huo unaonesha CCM imepokea ripoti ya Jaji Chande si kama nyaraka za kawaida za kisiasa, bali kama taarifa inayohitaji tathmini ya kina ya kitaifa. 

Ndiyo maana Migiro amesisitiza mara kadhaa kuwa ripoti hiyo imepokelewa kwa umakini mkubwa na kwamba chama kinataka kufahamu kwa undani nini kilitokea ili matukio hayo yasijirudie tena katika historia ya nchi.

Jambo jingine linalojitokeza ni kwamba CCM imeamua kuipa hadhi na heshima kubwa Tume ya Jaji Chande. Katika majibu yake, Dk.Migiro hajajaribu kubishana na takwimu zilizotolewa wala kuhoji uhalali wa kazi iliyofanywa na tume hiyo. 

Badala yake, amepongeza kazi ya tume, amewapongeza wananchi walioshiriki kutoa ushahidi na hata kusisitiza kuwa chama hakina sababu ya kutilia shaka vyanzo vya taarifa vilivyotumiwa kufikia hitimisho la ripoti hiyo. 

Binafsi niliamua kuifuatilia mahoajiano yake,nikawa makini kusikiliza maswali ya Kikeke lakini ukweli nilituliza akili yangu zaidi kusikiliza majibu ya Dk.Migiro ,mwanamama mbobebu katika siasa za kitaita na kimataifa.

Kupitia majibu ya Dk.Migiro nilibaini CCM imeamua kuikubali ripoti hiyo kama nyenzo muhimu ya kuelewa kilichotokea na kutafuta suluhisho la kudumu.

Aidha, majibu yake yanaonesha CCM imechagua kutenganisha masuala mawili makubwa yaliyokuwa yakijadiliwa na wananchi. Kwanza ni suala la kusikitishwa na vifo vya watu 518 vilivyotajwa katika ripoti. 

Pili ni suala la kutambua mchango wa vyombo vya ulinzi na usalama katika kuzuia hali isizidi kuwa mbaya zaidi. Migiro anajenga hoja kwamba inawezekana kukawa na makosa yaliyofanyika katika utekelezaji wa majukumu, lakini hilo haliondoi umuhimu wa kutambua jukumu la msingi lililofanywa na vyombo hivyo katika kulinda usalama na utulivu wa nchi wakati wa tukio hilo.

Katika eneo hilo ndipo unaonekana mkakati wa kisiasa wa CCM. Chama hakijakubali hoja kwamba pongezi zilizotolewa kwa vyombo vya ulinzi na usalama zilikuwa ni kufumbia macho madhara yaliyotokea. 

Badala yake, kinaeleza kuwa pongezi hizo zilihusu jukumu la jumla la kulinda utulivu wa taifa wakati uchunguzi wa kina kuhusu vifo na madhara mengine ukiendelea kufanyika kupitia mifumo ya kisheria.

Pia kuna ujumbe muhimu wa kisiasa ambao CCM inaonekana kuutuma kupitia Katibu Mkuu wake. Chama kinataka kuondoa taswira kwamba vyombo vya dola vinafanya kazi kwa ajili ya kukilinda CCM badala ya kulinda taifa. 

Katika majibu yake, Migiro anasisitiza kuwa kabla ya Oktoba 29 kampeni na shughuli za uchaguzi zilifanyika kwa utulivu nchini kote bila hitaji kubwa la kuingilia kati kwa vyombo vya usalama. 

Kwa mtazamo wa CCM, tukio la Oktoba 29 linaonekana kutazamwa zaidi kama changamoto ya kiusalama kuliko tukio la ushindani wa kisiasa.

Hata hivyo, swali gumu zaidi ambalo Migiro alikabiliana nalo ni kuhusu uwajibikaji. Hili ndilo eneo ambalo wananchi wengi wamekuwa wakisubiri kuona hatua za moja kwa moja baada ya ripoti ya Jaji Chande kutaja vifo na madhara mengine yaliyotokea. 

Badala ya kutaja watu binafsi wanaopaswa kuwajibika mara moja, Dk.Migiro amehamishia matumaini ya CCM kwenye tume ya uchunguzi wa jinai iliyoundwa kufuatilia kwa kina matukio hayo. 

Kauli hiyo inaonesha kuwa chama kinaamini uwajibikaji lazima ujengwe juu ya ushahidi wa kisheria na matokeo ya uchunguzi rasmi, badala ya maamuzi yanayotokana na shinikizo la kisiasa au hisia za wakati huo.

Kwa ujumla, majibu ya Dk. Migiro yanaonesha CCM imepokea ripoti ya Jaji Chande kwa njia tatu kuu. Kwanza, kama nyaraka muhimu ya kujifunza kilichotokea. Pili, kama msingi wa kutafuta namna ya kuzuia matukio kama hayo yasijirudie tena siku zijazo. 

Tatu, kama mwanzo wa mchakato wa uwajibikaji ambao chama kinaamini unapaswa kuongozwa na sheria, ushahidi na taasisi husika za uchunguzi.

Kwa mtazamo mpana zaidi, mahojiano hayo yanaashiria CCM imeamua kusimama katikati ya hoja mbili zinazovutana; upande mmoja kutetea uthabiti wa taasisi za dola na upande mwingine kukubali kuwa kuna maswali mazito yanayohitaji majibu kuhusu vifo na madhara yaliyotokea Oktoba 29. 

Huo ndio mwelekeo unaojitokeza katika namna viongozi wa chama walivyopokea, kutafakari na kuanza kuijadili hadharani ripoti ya Jaji Chande baada ya kipindi kirefu cha tathmini ya ndani ya chama.

Nihitimishe kwa kumpongeza Katibu Mkuu Dk.Asha-Rose Migiro kwa utulivu wake alipokuwa akijibu maswali ya Salim Kikeke,pili nampongeza Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Dk.Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayofanya katika kukisimamia na kukiongoza Chama hicho kwa utulivu mkubwa.

Pamoja na hayo nitoe rai kwa Watanzania wote kwa umoja wetu tunapaswa kutambua tunayo nafasi ya kuhakikisha tunailinda nchi yetu kwa wivu mkubwa.Umoja na mshikamano ndio silaha yetu.

Tumshukuru Mungu kwa kuendelea kutuweka katika mikono yake na hatimaye licha ya yale yaliyotokea Oktoba 29 kama

Taifa tumeendelea kuwa wamoja na shughuli zetu za uzalishaji zinaendelea.Kwa pamoja tuseme ahsante Mwenyezi Mungu muumba wa mbingu na aridhi na vyote vilivyomo.


Ukipiga tu nipomepokea kwani 

shida iko wapi mtu wangu

Simu 0713833822/0762451570

Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma


Mbunge wa Tunduru Kaskazini kupitia Chama cha ACT Wazalendo, Ado Shaibu, amewataka wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuepuka kuingiza siasa za uchaguzi mkuu wa mwaka 2030 katika mijadala ya Bunge, akisema hali hiyo inaweza kuathiri ubora wa majadiliano na utekelezaji wa majukumu muhimu ya chombo hicho.

Akichangia hoja ya Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha kwa mwaka wa fedha 2026/2027 leo Juni 2, 2026, Bungeni jijini Dodoma, Ado amesema Bunge ni taasisi muhimu inayopaswa kujadili masuala ya maendeleo kwa umakini bila kuruhusu ushindani wa kisiasa kutawala kila mjadala.

"Nafahamu siasa zinaendeshwa na siasa, na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni sehemu ambayo siasa haziwezi kuepukika. Hata hivyo, nawaomba wabunge wa CCM, homa ya kuelekea mwaka 2030 isiharibu mijadala ya Bunge hili," alisema.

Ameongeza kuwa ingawa siasa zina nafasi yake, kuzidisha mijadala ya kisiasa mapema kunaweza kuondoa mwelekeo wa Bunge katika kushughulikia masuala ya msingi yanayogusa maendeleo ya wananchi.

"Kuna ladha katika siasa, lakini tukizidisha chumvi mapema kiasi hiki, tutafika mahali ambapo hakuna wizara itakayoweza kujadiliwa kwa utulivu ndani ya Bunge. Mwenendo huo si mzuri kwa ustawi wa Bunge la Muungano wa Tanzania," alisisitiza.

Katika hatua nyingine, mbunge huyo aliipongeza Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kwa kazi iliyoifanya katika kupitia masuala ya fedha za Serikali, sambamba na kupongeza Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa kuendelea kusimamia uwajibikaji na matumizi sahihi ya fedha za umma.

Ado amesema mafanikio ya maendeleo ya taifa yanategemea uwajibikaji na usimamizi madhubuti wa rasilimali za umma, hivyo akaishauri Serikali kuendelea kuipatia Ofisi ya CAG rasilimali na fedha za kutosha ili iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi zaidi.

"Endapo tutaamua kuwa makini na kutekeleza wajibu wetu ipasavyo, nchi inaweza kufikia hatua kubwa zaidi za maendeleo. Ni muhimu Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali

(CAG)ikawezeshwa vya kutosha ili iendelee kufanya kazi yake kwa uhuru na ufanisi," amesema.

Kauli za Ado zimekuja wakati Bunge likiendelea kujadili bajeti za wizara mbalimbali kuelekea mwaka wa fedha 2026/2027.




Na mwandishi wetu, Morogoro

SERIKALI imeendelea kuimarisha mifumo ya uratibu, kujiandaa na kukabiliana na maafa ili kuhakikisha misaada ya kibinadamu inayotolewa inawafikia walengwa kwa wakati, ufanisi na kwa kuzingatia viwango vya kimataifa.

Hayo yameelezwa leo tarehe 02 Juni, 2026 na Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Usimamizi wa Maafa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Kanali Selestine Masalamado, wakati wa ufunguzi wa warsha ya zoezi la uigaji la uratibu wa utoaji wa misaada ya kibinadamu na usafirishaji wakati wa dharura, mkoani Morogoro.

Amesema utoaji wa misaada ya kibinadamu na usafirishaji wa dharura ni nguzo muhimu zinazowezesha kuokoa maisha ya wananchi walioathiriwa na maafa, kupunguza mateso ya waathirika na kuharakisha urejeshaji wa hali za kawaida katika maeneo yaliyoathirika.

“Kwa kutambua umuhimu huo, Serikali imeendelea kuimarisha mifumo ya uratibu, kujiandaa na kukabiliana na maafa kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ili kuhakikisha misaada inawafikia walengwa kwa wakati, ufanisi na kwa kuzingatia viwango vya kimataifa vya utoaji wa huduma za kibinadamu,” amesema.

Vilevile, amelishukuru Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP), washirika wote waliohusika katika utekelezaji wa Mradi wa Field-Based Preparedness Project (FBPP), ambapo katika kipindi cha miaka miwili iliyopita, mradi huo umechangia kwa kiasi kikubwa kuimarisha uwezo wa taifa katika sekta ya utoaji wa misaada ya kibinadamu na usafirishaji.

Amesema Tanzania imefanikiwa kuanzisha Kikosi Kazi cha Kitaifa cha Uratibu wa utoaji wa misaada ya kibinadamu na usafirishaji wa dharura mwezi Julai 2025, ambacho kimekuwa jukwaa muhimu la uratibu na ushirikiano baina ya taasisi za serikali na wadau wa kibinadamu.

“Zoezi hili la uigaji limeandaliwa kama jukwaa la kitaifa la kujifunza, kupima na kuboresha mifumo yetu ya uratibu wa shughuli za usafirishaji na utoaji wa misaada ya kibinadamu.”alieleza

Katika hatua nyingine, Kanali Masalamado amesisitiza umuhimu wa kuendelea kujumuisha masuala ya uhifadhi wa mazingira na ustahimilivu wa tabianchi katika mipango na shughuli za usafirishaji wa misaada ya kibinadamu ili kuhakikisha kuwa hatua tunazochukua leo hazisababishi changamoto mpya kwa vizazi vijavyo.

Naye Naibu Mkurugenzi wa Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) Bi. Christine Mendese amesema, Shirika hilo litaendelea kushirikiana na Serikali katika kukabiliana na changamoto za maafa kwa kutoa misaada ya kibinadamu ili kuwa na jamii stahimilivu dhidi ya majanga hususan katika kuzuia na kukabiliana na majanga mbalimbali.

Kwa upande wake Mratibu wa Maafa mkoa wa Pwani Bi.Roseline ameshukuru uwepo wa warsha hiyo itakayosaidia kuongeza uelewa katika masuala la utoaji wa misaada ya kibinadamu kwa waathirika wa maafa.

“Warsha hii imekuja wakati sahihi kwa kuzingatia mikoa ndiyo inaratibu masuala ya maafa kwa ngazi za Halmashauri zetu, tunashukuru kwa niaba ya ofisi ya mkoa kwa namna wadau mlivyoleta warsha hii na kutujengea uwezo, hii itaongeza tija katika masuala ya logistics wakati wa maafa na kusaidia kuwa na mwelekeo sahihi na kuepuka changamoto wakati wa kutekeleza majukumu ya logistics wakati wa maafa,” alisema Kimaro.









Na Pamela Mollel,Arusha

Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM anayeshughulikia Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Kenani Laban Kihongosi, anaanza ziara maalum ya siku tatu mkoani Arusha kuanzia Juni 4 hadi 6, 2026, kwa lengo la kusikiliza kero za wananchi, kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuimarisha uhai wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika ngazi zote

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Arusha, Katibu wa Itikadi, Siasa na Uenezi wa CCM Mkoa wa Arusha, Saipulani Ramsey, amesema ziara hiyo ni fursa adhimu kwa wananchi kufikisha changamoto zao moja kwa moja kwa viongozi wa chama na Serikali ili zipatiwe ufumbuzi wa haraka.

Ramsey amesema Kihongosi pamoja na ujumbe wake watatembelea na kukagua miradi mbalimbali inayotekelezwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, kwa lengo la kujionea maendeleo yaliyofikiwa na kupokea maoni ya wananchi kuhusu ubora wa huduma zinazotolewa

Ameeleza kuwa sekta za elimu, afya, maji na miundombinu ni miongoni mwa maeneo yatakayopata kipaumbele katika ziara hiyo, huku viongozi wakitarajiwa kukusanya maoni na mapendekezo yatakayosaidia kuboresha zaidi utoaji wa huduma kwa wananchi

Mbali na masuala ya maendeleo, ziara hiyo itahusisha tathmini ya uhai wa CCM kuanzia ngazi ya matawi hadi mkoa, pamoja na mikutano na wanachama na viongozi wa chama kwa ajili ya kujadili utekelezaji wa maelekezo mbalimbali ya chama.

Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa, Kihongosi ataanza ziara yake Wilaya ya Karatu Juni 4, kisha kuelekea Arumeru Juni 5, kabla ya kuhitimisha kwa mkutano mkubwa wa hadhara katika Jiji la Arusha Juni 6

Wakati huo huo, CCM Mkoa wa Arusha imesema imeendelea kuimarisha chama katika maeneo mbalimbali ambapo tayari imefikia kata 107 kati ya kata 161 kupitia ziara inayoongozwa na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Arusha, Thomas Ole Sabaya. Chama hicho kimesema mwitikio wa wananchi umekuwa mkubwa na umechangia kutatua changamoto mbalimbali za maendeleo katika jamii.




Na Mwandishi Wetu

TANZANIA imeshiriki kikao cha Kamati ya Utekelezaji wa Viwango vya Kazi kinachoendelea jijini Geneva, Uswisi, ikiwa ni sehemu ya Mkutano Mkuu wa 114 wa Shirika la Kazi Duniani (ILO).

Katika kikao hicho kilichifanyika leo Juni 2, 2026 ambapo wajumbe wamejadili masuala mbalimbali yanayohusu utekelezaji wa viwango vya kazi, ikiwemo mjadala wa jumla kuhusu ripoti kuu ya Kamati ya Mkutano na maadhimisho ya miaka 100 ya ajenda ya Kazi zenye Staha, Tathmini ya Jumla, pamoja na wajibu wa nchi wanachama katika kuwasilisha taarifa na kutekeleza majukumu mengine yanayohusiana na viwango vya kazi.

Ujumbe wa Tanzania katika kikao hicho ulijumuisha Jaji wa Mahakama ya Rufani Dkt. Yose Joseph Mlyambina, Kamishna wa Kazi kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Kazini, Suzan Mkangwa, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali Pa Kazi (OSHA), Khadija Mwenda, pamoja na Mkurugenzi wa Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA), Usekelege Mpulla

Tanzania, ambayo ni mwanachama wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) na mjumbe wa Bodi ya Magavana inayowakilisha nchi za Ukanda wa Afrika Mashariki, inaendelea kushiriki Mkutano Mkuu wa 114 wa shirika hilo unaowakutanisha wawakilishi wa Serikali, Waajiri na Wafanyakazi kutoka nchi wanachama 187.





Na Mwandishi Wetu


MAHAKAMA Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, imewahukumu kifungo cha maisha jela Suleiman Thabit Ngulangwa na Farid Hamis Said baada ya kutiwa hatiani kwa kosa la biashara haramu ya dawa za kulevya aina ya heroin yenye uzito wa kilo 15.19.

Katika hukumu iliyotolewa Juni 1, 2026, Jaji S.E. Kisanya alisema ushahidi wa upande wa mashtaka ulithibitisha pasipo shaka kuwa washtakiwa hao walikuwa na umiliki wa dawa hizo.

Mchambuzi wa Serikali kutoka Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali (GCLA), Leonida Daniel Michael, aliithibitishia mahakama kuwa pakiti 16 zilizokamatwa zilikuwa na heroin yenye uzito wa kilo 15.19 baada ya kufanyiwa uchunguzi wa kisayansi.

Mahakama ilibaini kuwa utetezi wa washtakiwa haukuweza kuibua shaka dhidi ya ushahidi wa mashahidi na vielelezo vilivyowasilishwa.

Mshtakiwa wa pili, Sharifa Selemani Bakari, aliachiliwa huru baada ya mahakama kubaini kuwa upande wa mashtaka haukuthibitisha ushiriki wake katika kosa hilo.

Mbali na kifungo hicho, mahakama imeagiza heroin yote iliyokamatwa pamoja na vifaa vya kufungashia kuteketezwa kwa mujibu wa sheria.




Na Mwandishi Wetu, DODOMA

Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Mwaka 2026 umezindua mradi wa kusimika kamera za usalama wenye thamani ya shilingi 682,561,548.6, ukiwa na lengo la kuimarisha ulinzi na usalama wa raia, mali zao pamoja na miundombinu ya umma.

Mradi huo umetekelezwa kwa ushirikiano ambapo Halmashauri ya Jiji la Dodoma imetoa kiasi cha shilingi 519,891,609.27, huku Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) ukichangia shilingi 162,669,939.34 kupitia Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) kwa ajili ya kuunganisha mfumo huo kupitia Mkongo wa Taifa.

Akizungumza mara baada ya kukagua mradi huo, Wazo Mwang’onda alisema ameridhishwa na mradi huo katika kuimarisha usalama wa Jiji la Dodoma na utasaidia kuvutia wawekezaji kutokana na mazingira salama yaliyopo.

“Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amewahakikishia wawekezaji usalama wao kwa kuonesha dhamira ya serikali kwa kutenga fedha nyingi kwa ajili ya kufunga kamera katika Jiji la Dodoma. 

Dodoma iko salama, na uhalifu wowote utakaojitokeza utashughulikiwa kwa mujibu wa taratibu za Jeshi la Polisi kwa haraka, kwa kuwa wahalifu wataweza kufuatiliwa kwa urahisi kupitia mfumo huu. Mwenge wa Uhuru umefurahishwa na ufungaji wa kamera hizi kwa ajili ya kuimarisha usalama” alisema Mwang’onda.

Akisoma taarifa ya mradi huo, Mkuu wa Kitengo cha TEHAMA, Joseph Fungo alisema kuwa mradi huo umekamilika kwa asilimia 80, ukihusisha kusimika nguzo, kufunga kamera pamoja na vifaa katika chumba cha kuongozea. 

Alieleza kuwa hatua zinazofuata ni kuunganisha kamera zote ili ziweze kusomana na chumba cha kuongozea kupitia Mkongo wa Taifa, kuingiza umeme wa gridi katika vituo 33 vya kamera, kutoa mafunzo kwa watumiaji, na kuandaa mfumo wa usimamizi katika kipindi cha matazamio.

Nae, Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma, Alimwoni Chaula alisema kuwa wamejifunza kutoka nchi mbalimbali na kubaini kuwa usalama ni nguzo muhimu katika miji ya kisasa. Aliongeza kuwa kamera za ulinzi barabarani zitasaidia kudhibiti matukio ya uhalifu hali inayowapa wawekezaji uhakika zaidi wa mazingira salama.






Na Benny Mwaipaja, Dodoma.

Serikali kupitia Wizara ya Fedha imeliomba Bunge kuidhinisha jumla ya shilingi trilioni 21.3 kwa ajili ya utekelezaji wa majukumu ya Wizara hiyo pamoja na taasisi zake kwa Mwaka wa Fedha 2026/27.

Akiwasilisha Mapendekezo ya Mpango na Bajeti bungeni, Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), alisema fedha hizo zitatumika kugharamia matumizi ya kawaida na maendeleo katika mafungu manane ya Wizara, ambapo kati ya fedha hizo, shilingi trilioni 19.4 zitatumika kwa matumizi ya kawaida huku shilingi trilioni 1.8 zikielekezwa kwenye miradi ya maendeleo.

Alisema kuwa katika Bajeti hiyo, Serikali imepanga kuendelea kusimamia uchumi kwa weledi ili kuhakikisha ukuaji wa uchumi unafikia asilimia 6.3 mwaka 2026 huku mfumuko wa bei ukidhibitiwa kubaki katika katika wigo wa wastani wa asilimia 3 hadi 5.

“Serikali pia inalenga kuimarisha nidhamu ya matumizi ya fedha za umma pamoja na kuongeza ufanisi wa ukusanyaji wa mapato ya ndani” alisema Mhe. Balozi Omar.

Aidha, alibainisha kuwa Wizara imepanga kutenga shilingi bilioni 100 kila mwezi kwa ajili ya kulipa madeni ya watumishi, wakandarasi, wazabuni na watoa huduma ili kupunguza changamoto za malimbikizo ya madeni serikalini.

Kwa upande wa mapato, alisema kuwa Wizara ya Fedha imekadiriwa kukusanya jumla ya shilingi trilioni 55.2, ambapo Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) inatarajiwa kukusanya zaidi ya shilingi trilioni 39.

Katika hatua nyingine, aliliomba Bunge kuiidhinishiwa Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi shilingi bilioni 132.2 kwa ajili ya kuimarisha shughuli za ukaguzi wa matumizi ya fedha za umma pamoja na kuendelea na ujenzi wa ofisi zake katika baadhi ya mikoa nchini.

Mhe. Balozi Omar alieleza kuwa bajeti hiyo imeandaliwa kwa kuzingatia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa pamoja na Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.


TATHMINI YA UTEKELEZAJI WA BAJETI YA 2025/26


Mhe. Balozi Omar alieleza kuwa jumla ya shilingi trilioni 20.18 ziliidhinishwa kwa ajili ya utekelezaji wa matumizi ya kawaida na maendeleo kwa mafungu manane ya wizara hiyo katika mwaka wa fedha 2025/26.

Alisema kati ya fedha hizo, shilingi trilioni 19.43 zilitengwa kwa matumizi ya kawaida ikijumuisha mishahara ya shilingi trilioni 1.10 na matumizi mengineyo ya shilingi trilioni 18.33.

“Bajeti ya maendeleo ilikuwa shilingi bilioni 747.30, ambapo shilingi bilioni 601.70 zilikuwa fedha za ndani na shilingi bilioni 145.60 fedha za nje” Alisema Mhe. Balozi Omar.

Alisema kuwa wakati wa mapitio ya kati ya mwaka, bajeti ya wizara ilihuishwa na kupungua kutoka shilingi trilioni 20.18 hadi shilingi trilioni 19.94, ambapo kati ya kiasi hicho, shilingi trilioni 19.45 zilitengwa kwa ajili ya matumizi ya kawaida na shilingi bilioni 485.99 kwa ajili ya miradi ya maendeleo.

“Hadi kufikia mwisho wa Aprili 2026, wizara ilikuwa imepokea jumla ya shilingi trilioni 14.08 sawa na asilimia 70.63 ya bajeti iliyohuishwa. Matumizi halisi yalifikia shilingi trilioni 14.05, sawa na asilimia 99.76 ya fedha zilizopokelewa” alifafanua Mhe. Balozi Omar.

Wizara pia ilieleza mafanikio yaliyopatikana katika ukusanyaji wa mapato, usimamizi wa deni la Serikali pamoja na ukuaji wa uchumi ambapo katika kipindi cha Julai 2025 hadi Aprili 2026, Serikali ilifanikiwa kukusanya na kutafuta shilingi trilioni 41.37 kutoka vyanzo vya ndani na nje, sawa na ufanisi wa asilimia 82.4 ya lengo la mwaka.

Katika kipindi hicho, Serikali ilitumia shilingi trilioni 9.74 kuhudumia deni la Serikali, ambapo shilingi trilioni 4.45 zilielekezwa kwenye deni la nje na shilingi trilioni 5.29 kwa ajili ya deni la ndani na kwamba ulipaji wa madeni kwa wakati umeendelea kuijengea Tanzania imani katika masoko ya fedha ya kikanda na kimataifa.

“Nina furaha kulijulisha Bunge lako Tukufu kuwa Tanzania imeibuka mshindi wa jumla katika Tuzo ya Usimamizi wa Deni la Umma katika nchi za Jumuiya ya Madola, pamoja na tuzo ya Ofisi Bora ya Usimamizi wa Deni la Serikali katika Kanda ya Afrika” alisisitiza Mhe. Balozi Omar.

Kwa upande wa uchumi, Tanzania ilikua kwa wastani wa asilimia 5.9 mwaka 2025 ikilinganishwa na asilimia 5.5 mwaka 2024. Ukuaji huo umechangiwa na kuongezeka kwa mikopo kwa sekta binafsi, kuimarika kwa miundombinu, shughuli za kilimo, uchimbaji madini, ujenzi pamoja na utekelezaji wa miradi ya kimkakati.

Aidha, alieleza kuwa kiwango cha mfumuko wa bei kiliendelea kubaki katika wastani wa asilimia 3.4 huku akiba ya fedha za kigeni ikifikia dola za Marekani bilioni 5.723, kiasi kinachotosheleza uagizaji wa bidhaa na huduma kutoka nje kwa zaidi ya miezi 4.4

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akiwasilisha bungeni jijini Dodoma, Mapitio ya Utekelezaji wa Mpango na Bajeti kwa mwaka wa fedha 2025/2026 na Mapendekezo ya Mpango na Bajeti ya Wizara ya Fedha kwa mwaka 2026/2027, ambapo ameliomba Bunge kuidhinisha jumla ya shilingi trilioni 21.3 kwa ajili ya utekelezaji wa majukumu ya Wizara pamoja na taasisi zake kwa Mwaka wa Fedha 2026/27. (Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Dodoma)
NALA - DODOMA

‎HALMASHAURI ya Jiji la Dodoma imetekeleza ujenzi wa barabara ya lami yenye urefu wa kilomita 1.6 kutoka barabara kuu ya Bahi hadi Hospitali ya Jiji, hatua inayolenga kuboresha huduma za afya na kiuchumi kwa wananchi wa Kata ya Nala.

‎Akizungumza wakati wa uzinduzi wa barabara hiyo, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Mwaka 2026, Wazo Mwang’onda alipongeza mradi huo na kusema kuwa ni bora, umekidhi vigezo vyote muhimu kama taratibu za ujenzi wa barabara ya kiwango cha lami zinavyotaka.

‎Alisema kuwa Mwenge wa Uhuru umeridhishwa na ujenzi huo na upo tayari kuizindua. “Mwenge wa Uhuru umeridhishwa na ujenzi huu wa barabara ya Kilomita 1.6 ambayo imekamilika kwa ubora wa hali ya juu na sasa upo kwenye matazamio ya mwisho, umeridhishwa na namna barabara hii imejengwa. Tunaamini wakazi wa eneo hili watanufaika sana na uwepo wa barabara hii" alisema Mwang’onda.

‎Awali akisoma taarifa ya mradi wa ujenzi wa barabara hiyo, Mhandisi wa Miradi katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Mha. Nicodemus Kileo alisema kuwa mradi huo ulitekelezwa na mkandarasi mzawa M/s. Kings Builders Limited kwa gharama ya shilingi bilioni 2.87 zilizotokana na mapato ya ndani ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma, na upo tayari kuzinduliwa.

‎Nae, Mkazi wa Nala, Gervazi Sebastian alipongeza ujenzi wa barabara hiyo akieleza kuwa imeondoa adha ya usafiri kwa wakazi wa Nala. "Tunaishukuru sana serikali kwa kutujengea hii barabara, awali ilikuwa ngumu kupata usafiri wa nafuu kwasababu barabara ilikua mbovu. Kwakweli serikali imetuokoa hata huduma zingine zinapatikana kwa urahisi" alisema Sebastian.

‎Katika hatua nyingine, Mkazi wa Mtaa wa Segu Chini, Asia Omari alipongeza ujenzi wa barabara hiyo akisema kuwa imekuwa mkombozi kwa watumiaji hasa wanawake wajawazito wanaopita kwenda kupata matibabu katika Hospitali ya Jiji la Dodoma.

‎Mradi huo ni miongoni mwa miradi iliyozinduliwa na kuwekewa jiwe la msingi na Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Mwaka 2026 uliobeba kaulimbiu isemayo “Tanzania ni Yetu Sote, Tushikamane kwa Pamoja Kuleta Maendeleo”.





Top News