-Asilimia 80 ya Mizigo Inaingia Tanzania Kwa Njia ya Maji
NA MWANDISHI WETU, KIGOMA
WAZIRI wa Uchukuzi, Profesa Makame Mnyaa Mbarawa, amesema mabaharia ni nguzo muhimu ya usafirishaji duniani na walinzi wakuu wa mnyororo wa biashara na uchumi, hivyo wanapaswa kuendelea kupewa mazingira bora ya kazi, mafunzo na fursa za maendeleo ili kuongeza mchango wao katika uchumi wa taifa.
Profesa Mbarawa ametoa kauli hiyo wakati wa kilele cha Maadhimisho ya 16 Siku ya Mabaharia Duniani yaliyofanyika mkoani Kigoma.
Alisema zaidi ya asilimia 80 ya biashara ya dunia husafirishwa kwa njia ya maji, jambo linalowafanya mabaharia kuwa mhimili muhimu wa uchumi wa kimataifa licha ya kukabiliwa na changamoto mbalimbali wanazokutana nazo ikiwemo kukaa muda mrefu baharini, kutengana na familia zao, mazingira magumu ya kazi na hatari za kiusalama, bado wanaendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi na kujitolea.
“Mabaharia ndio uti wa mgongo wa sekta ya usafirishaji duniani. Kazi yao inahakikisha bidhaa muhimu zinafika kwa wakati na uchumi wa dunia unaendelea kuzunguka. Tunawapongeza kwa moyo wao wa kujitolea na uzalendo,” alisema.
Amesema kauli mbiu ya maadhimisho hayo inapaswa kutekelezwa kwa vitendo kupitia sera madhubuti, utoaji wa mafunzo ya kisasa na kuimarisha ushirikiano wa kimataifa ili kuhakikisha sekta ya usafiri majini inakua sambamba na mahitaji ya dunia ya sasa.
“Mabaharia ni mhimili mkubwa wa uchumi wa dunia. Tunapaswa kuhakikisha wanapatiwa mafunzo yanayoendana na mabadiliko ya teknolojia na mazingira ya kazi ili waweze kukabiliana na kasi ya mabadiliko yanayotokea duniani,” amesema Profesa Mbarawa.
Ameeleza kuwa maadhimisho ya mwaka huu yanaenda sambamba na juhudi za Serikali za kuongeza uwekezaji katika shughuli za usafirishaji na uchumi wa bluu, hatua ambayo imeendelea kufungua fursa nyingi za ajira kwa vijana na wanawake.
Kwa mujibu wa Waziri huyo, ongezeko la ajira katika sekta ya usafiri majini linaendana na malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kukuza uchumi, kuongeza uzalishaji na kuboresha maisha ya wananchi.
Aidha, amesema Tanzania na Uganda zimeingia katika makubaliano ya ushirikiano wa shughuli za utafutaji na uokoaji majini, huku akieleza kuwa utekelezaji wa sheria na mifumo ya utafutaji na uokoaji utasaidia kuimarisha usalama wa mabaharia, abiria na vyombo vya usafiri majini.
Profesa Mbarawa amewataka mabaharia kuendelea kuwa waadilifu, kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za kazi pamoja na kutoa taarifa kwa mamlaka husika pindi wanapobaini changamoto zinazoweza kuhatarisha usalama wa vyombo na watu.
Amesema maadhimisho hayo yamekuwa jukwaa muhimu la utoaji elimu, kubadilishana uzoefu na kutoa maelekezo yatakayosaidia kukuza sekta ya usafiri wa majini nchini.
Katika hatua nyingine, ameliagiza Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) kuharakisha utekelezaji wa mikakati ya kuwatafutia mabaharia wa Tanzania fursa zaidi za ajira katika soko la kimataifa, huku akisisitiza umuhimu wa kuwapa wanawake kipaumbele katika ajira za sekta hiyo.
Pia ameitaka TASAC kukamilisha kanzidata ya mabaharia nchini pamoja na kufanya tathmini ya mifumo ya maslahi yao ili kuhakikisha ustawi wa mabaharia unaimarishwa na changamoto zao zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati.
Vilevile, ameshauri TASAC kuendelea kufanya mazungumzo na wamiliki wa meli mbalimbali ili waweze kufungua ofisi zao nchini Tanzania hatua itakayorahisisha upatikanaji wa ajira kwa mabaharia wa Kitanzania na kuongeza ushindani wao katika soko la kimataifa.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa TASAC Mohamed Salum amesema kuwa TASAC imesaini mikataba mbalimbali ya Kimataifa hatua ambayo itasaidia kuongeza uwigo wa ajira kwa mabaharia.
Amesema kuwa Serikali imefanya uwekazaji katika bandari ambapo fursa zimeongezeka kwa mabaharia pamoja kuendelea kuratibu katika mfumo kwa mabaharia kuwa kwenye mfumo huo.
Aidha amesongeza kuwa TASAC imenunua Boti za uokozi ili kuhakikisha wananchi na mabaharia wanakuwa salama wakati wote na wakipata majanga wanaokolewa.
Waziri wa Uchukuzi Profesa Makame Mnyaa Mbarawa (MB)akifunga maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma
Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa ,Mkuu wa Wilaya ya Kigoma Dkt.Rashid Chuachua akizungumza wakati wa kumkaribisha mgeni rasmi katika Kilele cha maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma.
Mwenyekiti wa Bodi ya TASAC Nah.Mussa Mandia akitoa maelezo katika kilele cha maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma.
Mkurugenzi Mkuu wa TASAC Mohamed Salum akitoa maelezo kuhusiana na umhimu wa mabaharia katika maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma.
Mkuu wa Chuo cha DMI Profesa Tumain Gurumo akizungumza katika kilele cha maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma.
Picha za makundi mbalimbali katika kilele katika maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma.