Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi (kulia) akizungumza jambo wakati wa kikao chake na wawakilishi wa Ubalozi wa Uingereza nchini Tanzania uliongozwa na Kiongozi wa Programu Endelevu ya Mazingira kutoka Ubalozi wa Uingereza Nchini Tanzania, Bw. Euan Davidson. Kikao hicho kilifanyika katika Ofisi ndogo ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Luthuli Jijini Dar es Salaam leo Alhamisi Machi 05, 2026.

*****************

Serikali imesema itaendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo ili kuhakikisha vipaumbele vya Ajenda ya Mazingira na Mabadiliko ya Tabianchi vinapewa msukumo katika majukwaa ya Kitaifa na Kimataifa.

Hayo yamesemwa leo Jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Richard Muyungi wakati wa mazungumzo baina yake naKiongozi wa Programu Endelevu ya Mazingira kutoka Ubalozi wa Uingereza nchini Tanzania, Bw. Euan Davidson.

Dkt. Muyungi amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Rais Dkt, Samia Suluhu Hassan imeweka mikakati na mipango mahsusi ya kitaifa kuhusu masuala ya mazingira na tabianchi ambayo inahitaji msukumo na ushirikiano wa karibu na wadau wa maendeleo.

Ameitaja mikakati hiyo ni pamoja na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ambapo nguzo ya tatu inaelezea kuhusu masuala ya uhifadhi wa mazingira na ustahimilivu dhidi ya mabadiliko ya tabianchi, juhudi zinazolenga kuiwezesha Tanzania kufikia nchi ya kipato cha kati ngazi ya juu ifikapo 2050.

Aidha Dkt. Muyungi amesema kipaumbele kingine kilichopewa msukumo ni pamoja na biashara ya kaboni, ambapo Serikali imeweka mazingira wezeshi kwa wadau na kwakuandaa utaratibu wa kitaifa na kimataifa kwa kuanzisha Kituo cha Taifa cha Kufuatilia Kaboni (NCMC).

“Tanzania tayari ina kanuni na miongozo ya biashara ya kaboni na Kituo cha NCMCtayari kimeanza kazi kikiwa na bodi ya wakurugenzi na kamati ya wataalamu ya uchambuzi wa miradi ya kaboni” asema Dkt. Muyungi.

Dkt. Muyungi ametaja kipaumbele kingine cha Serikali kupitia hifadhi ya mazingira ni pamoja na mkakati wa kuhamasisha jamii kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia ambapo kinara wa kampeni hiyo kitaifa na kimataifa ni Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muunganio wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Akifafanua zaidi, Dkt. Muyungi ameeleza kuwa Tanzania pia inaendelea na utekelezajina Mchango wa tatu wa kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi (NDC 3) ambao umeandaliwa kwa ajili ya kupunguza uzalishaji wa gesi joto na kujenga ustahimilivu wa mazingira.

Kwa upande wake, Kiongozi wa Programu Endelevu ya Mazingira kutoka Ubalozi wa Uingereza Nchini Tanzania, Bw. Euan Davidson amesema Ubalozi huo upo tayari kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais ili kufanikisha ajenda ya mazingira na mabadiliko ya tabianchi.

“Tupo tayari kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais katika masuala ya Uchumi wa Buluu, biashara ya kaboni, teknolojia ya nishati safi ya kupikia na ukamilishwaji wa mchango wa taifa wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi” amesema Bw. Davidson.
Kiongozi wa Programu Endelevu ya Mazingira kutoka Ubalozi wa Uingereza nchini Tanzania, Bw. Euan Davidson (kushoto) akizungumza jambo na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Richard Muyungi wakati wa mazungumzo baina yao yaliyofanyika katika Ofisi ndogo ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Luthuli Jijini Dar es Salaam leo Alhamisi Machi 05, 2026.
Mshauri wa masuala ya mazingira kutoka Ubalozi wa Uingereza Bw. Abdallah Shaha(kulia) akizungumza jambo wakati wa kikao baina ya Ubalozi huo na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi kilichofanyika katika Ofisi ndogo za Ofisi ya Makamu wa Rais, Luthuli Jijini Dar es Salaam leo Alhamisi Machi 05, 2026.
`
Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi akizungumza jambo wakati kikao chake na wawakilishi wa Ubalozi wa Uingereza uliongozwa Kiongozi wa Programu Endelevu ya Mazingira kutoka Ubalozi wa Uingereza Nchini Tanzania, Bw. Euan Davidson. Kikao hicho kilifanyika katika Ofisi ndogo ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Luthuli Jijini Dar es Salaam leo Alhamisi Machi 05, 2026.


Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi akiwa katika picha ya pamoja na Kiongozi wa wa Programu Endelevu ya Mazingira kutoka Ubalozi wa Uingereza nchini Tanzania, Bw. Euan Davidson muda mfupi baada ya kumalizika kwa mazunngumzo baina yao yaliyofanyika katika Ofisi ndogo za Ofisi ya Makamu wa Rais, Luthuli Jijini Dar es Salaam leo Alhamizi Machi 05, 2026.

Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi akiwa katika picha ya pamoja na wawakilishi wa Ubaloziw a Uingereza nchini Tanzania muda mfupi baada ya kumalizika kwa mazunngumzo baina yao yaliyofanyika katika Ofisi ndogo za Ofisi ya Makamu wa Rais, Luthuli Jijini Dar es Salaam leo Alhamizi Machi 05, 2026.

(NA MPIGAPICHA WETU)
Mkutano Maalumu wa 59 wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) umefanyika leo tarehe 5 Machi 2026 jijini Arusha, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya mwisho ya Mkutano wa 25 wa Wakuu wa Nchi wanachama wa Jumuiya hiyo utakaofanyika tarehe 7 Machi 2026.

Mkutano huo ambao umepokea na kujadili taarifa ya kikao cha Makatibu Wakuu, pamoja na masuala mengine umekamilisha maandalizi ya ajenda zitakazojadiliwa na kutolewa maamuzi pamoja na maelekezo na Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa EAC, ambao ndio chombo cha juu cha maamuzi ndani ya Jumuiya hiyo.

Akizungumza katika ufunguzi wa mkutano huo Mhe. Beatrice Askul Moe Waziri anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki Kenya na Mwenyekiti wa Mkutano huo ameeleza kuwa ajenda zilizoandaliwa zitatoa mwelekeo mpya wa utatuzi wa changamoto mbalimbali zinazoikabili Jumuiya kwa sasa ikiwemo uhaba wa rasilimali fedha za kuendesha shughuli mbalimbali za Sekretariati ya EAC na upungufu wa wafanyakazi.

Aidha, ametoa rai kwa wajumbe wa mkutano huo kuendelea kuimarisha na kudumisha ushirikiano uliopo katika Jumuiya, huku akibainisha kuwa kutokana na ushirikiano huo umeziwezesha nchi Wanachama kuweza kuhimili misukosuko inayosababishwa na kuyumba kwa uchumi wa dunia ikiwemo ongezeko la bei za bidhaa muhimu kama vile chakula.

Miongoni mwa ajenda muhimu zinazotarajiwa kuwasilishwa na kujadiliwa katika mkutano huo wa 25 wa Wakuu wa Nchi ni pamoja na maendeleo ya utekelezaji wa Itifaki ya Soko la Pamoja la EAC, kuondolewa kwa vikwazo visivyo vya ushuru (Non-Tariff Barriers – NTBs), kukubaliana kuhusu kanuni ya uchangiaji wa michango ya Jumuiya, pamoja na kuimarisha ushirikiano katika sekta za utalii, miundombinu na nishati.

Kwa sasa, Jumuiya ya Afrika Mashariki inaundwa na nchi wanachama nane ambazo ni Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Sudan Kusini, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) na Somalia, ikiwa na jumla ya idadi ya watu inayokadiriwa kufikia zaidi ya milioni 300 na pato la pamoja la uchumi (GDP) linalokadiriwa kuzidi dola za Marekani bilioni 300.

Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo umeongozwa na Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, ukijumuisha Naibu Mawaziri kutoka sekta mbalimbali wakiwemo; Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde Naibu Waziri Fedha, Mhe. Regina Ndege Qwaray, Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora na Mhe. Dennis Lazaro Londo Naibu Waziri Viwanda na Biashara na Viongozi wengine Waandamizi wa Serikali.













Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), Dkt. Prosper Mgaya, amesema kuna umuhimu mkubwa wa kuongeza ushiriki wa watoto wa kike katika masomo ya sayansi na uhandisi ili kuwapa fursa sawa katika taaluma hizo muhimu kwa maendeleo ya nchi.

Dkt. Mgaya ameyasema hayo wakati wa ziara ya wanafunzi wa Shule ya Sekondari Tuliani iliyopo Magomeni walipotembelea chuoni hapo kwa lengo la kujifunza na kujionea mazingira halisi ya masomo ya sayansi na uhandisi yanavyotolewa.

Amesema chuo hicho kwa kushirikiana na Benki ya Dunia kinaendelea kutekeleza mradi wa kuanzisha Kituo cha Umahiri cha masuala ya usafiri wa anga, ambacho kitakuwa na majengo pamoja na vifaa vya kisasa vinavyofanana na vile vinavyopatikana katika vyuo vikuu vya kimataifa.

Kwa mujibu wa Dkt. Mgaya, ziara ya wanafunzi hao imelenga kuwapa fursa ya kuona kwa vitendo mazingira ya kujifunzia pamoja na vifaa vinavyotumika katika taaluma za urubani na matengenezo ya ndege, ili kuwasaidia kupata mwamko na uelewa kuhusu fursa zilizopo nchini katika masomo ya sayansi na uhandisi.

Amefafanua kuwa takwimu zinaonesha ushiriki wa watoto wa kike katika kozi za sayansi na uhandisi bado ni mdogo, ambapo kwa sasa hauzidi asilimia 15, licha ya uwezo mkubwa wanafunzi wa kike wanaouonesha wanapopata nafasi ya kusoma masomo hayo.

Ameongeza kuwa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imekuwa ikiendesha programu mbalimbali za kuhamasisha watoto wa kike kujikita katika masomo ya sayansi, huku NIT pia ikiendelea kutembelea shule mbalimbali nchini kutoa uelewa kuhusu fursa za masomo hayo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Shule ya Sekondari Tuliani, Happiness Mailo, amesema ziara hiyo imekuwa na manufaa makubwa kwa wanafunzi, hasa wa kike, kwa kuwa imewapa fursa ya kuona kwa vitendo mazingira ya masomo ya sayansi na uhandisi na hivyo kuwajengea hamasa ya kuyachagua katika masomo yao ya baadaye.

Amesema wanafunzi wengi wa kike hukata tamaa mapema kutokana na dhana potofu kuwa masomo ya sayansi ni magumu, hivyo ziara kama hizo husaidia kubadilisha mtazamo huo na kuwahamasisha kujiamini zaidi katika masomo yao.

Naye mwanafunzi wa kidato cha pili katika Shule ya Sekondari Tuliani, Lissa Ramadhani, amesema ziara hiyo imewasaidia kufahamu zaidi kuhusu taaluma za sayansi na uhandisi ambazo awali waliziona kuwa ngumu au zisizowahusu.

Amehimiza wanafunzi wengine wa kike kuondoa hofu na kujiamini katika kusoma masomo ya sayansi, akisema kuwa fursa za taaluma hizo ni nyingi na zina mchango mkubwa katika maendeleo ya taifa.










Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kupitia Kanda ya Kaskazini, leo tarehe 5 Machi 2026 imetoa elimu kwa viongozi wa Wilaya ya Korogwe katika semina iliyofanyika katika ukumbi wa GMCC.

Akimkaribisha Mgeni Rasmi, Meneja wa EWURA Kanda ya Kaskazini, George Mhina, alisema lengo ni kuwajengea viongozi uelewa kuhusu majukumu ya EWURA na maeneo inayoyadhibiti ili kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Katika semina hiyo, washiriki walipatiwa elimu kuhusu umuhimu wa uvunaji wa maji ya mvua, matumizi ya nishati safi ya kupikia, leseni za mafundi umeme, ujenzi wa vituo vya mafuta vijijini pamoja na namna ya kutatua migogoro katika sekta za maji na nishati.

Akizungumza katika kikao hicho, Mkuu wa Wilaya ya Korogwe Mhe. William Mwakilema amewasisitiza viongozi hao kuwa mabalozi wa elimu waliyoipata kwa kuhakikisha wanaifikisha kwa wananchi ili kuongeza uelewa na matumizi sahihi ya huduma za maji na nishati.

 

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Kuelekea maadhimisho ya miaka 25 ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), Mkurugenzi wa chuo hicho Kampasi ya Dar es Salaam, Mussa Lugembe, amewataka wanafunzi wa vyuo na shule za sekondari kuwa waadilifu na wazalendo ili kujenga msingi imara wa utumishi wa umma wenye uwajibikaji nchini.

Lugembe alitoa wito huo alipokuwa akizungumza na wanafunzi wa Shule ya Sekondari Azania jijini Dar es Salaam, ambapo alisema chuo hicho kimeanza kutoa elimu ya maadili na uzalendo kwa vijana ili kuwajengea uelewa mapema kuhusu misingi ya utumishi wa umma kabla hawajaingia rasmi katika ajira za serikali.

Alieleza kuwa lengo la mpango huo ni kuwaandaa watumishi wa umma wa baadaye wanaotambua wajibu wao kwa taifa, wanaozingatia maadili ya kazi, uwajibikaji na uzalendo wanapokuwa katika nafasi mbalimbali za utumishi wa umma.

“Tunataka vijana waanze kujifunza mapema kuhusu maadili ya utumishi wa umma ili wanapopata nafasi za ajira wawe tayari kulitumikia taifa kwa uadilifu, uwajibikaji na uzalendo,” alisema Lugembe.
Kwa upande wake, Mkuu wa Shule ya Sekondari Azania, Melsius Kayombo, aliipongeza TPSC kwa kuandaa programu hiyo ya utoaji elimu kwa wanafunzi akisema itawasaidia kujenga misingi imara ya maisha na kuwalea kuwa viongozi na watumishi wa umma wenye maadili katika siku zijazo.

Naye mwanafunzi wa Azania, Faidh Mussa, alisema elimu hiyo imewasaidia wanafunzi kuelewa umuhimu wa uzalendo, uwajibikaji na maadili katika kujenga taifa lenye maendeleo.

Kwa upande wake, mwanafunzi wa Chuo cha Utumishi wa Umma, Mwishehe Ming’uno, alisema mafunzo hayo yanawapa motisha wanafunzi kuzingatia maadili ya kazi na kujiandaa kuwa watumishi wa umma watakaolitumikia taifa kwa ufanisi na uadilifu.

Aidha, Lugembe alibainisha kuwa katika kuadhimisha miaka 25 ya chuo hicho, Kampasi ya Dar es Salaam tayari imeshatembelea shule mbalimbali jijini Dar es Salaam ikiwemo Benjamin Mkapa, Jangwani, Tambaza na Azania, kwa lengo la kutoa elimu kuhusu maadili, uzalendo na umuhimu wa kuwajibika kwa taifa.












 

Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimeongoza Kikao cha 12 cha Makatibu Wakuu wa Vyama vya Ukombozi Kusini mwa Afrika, ambapo, pamoja na mambo mengine, vimejadili hali ya siasa, ukombozi wa kiuchumi na kuboresha hali za wananchi katika nchi zao. 

Kikao hicho kilichofanyika leo tarehe 5 Machi 2026, Kibaha, mkoani Pwani, kilihusisha Makatibu Wakuu wa Vyama 6 vya Ukombozi Kusini mwa Afrika, ambavyo ni ANC (Afrika Kusini), CCM (Tanzania), FRELIMO (Msumbiji), SWAPO (Namibia), ZANU-PF (Zimbabwe) na MPLA (Angola).

Akizungumza na vyombo vya habari baada ya mkutano huo, Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi, Asha-Rose Migiro, amesema kuwa katika kikao hicho wamepitia maazimio ya Mkutano Mkuu wa Wakuu wa Vyama hivyo uliofanyika mwaka jana, nchini Afrika ya Kusini. 

Alisema mijadala ilijikita kuangalia hali ya kisiasa katika ukanda wa Kusini mwa Afrika, hususan kulinda uhuru wa kisiasa na kiuchumi, kutathmini malengo ya harakati za ukombozi pamoja na kuendelea kulinda na kuimarisha uhuru uliopatikana.

Dkt. Migiro amesema jukumu kubwa la vyama hivyo ni kuimarisha mshikamano na umoja wao pamoja na kujadili changamoto mbalimbali zinazoikabili kanda hiyo ikiwemo mabadiliko ya tabianchi. Aidha, walijadili namna ya kutatua migogoro katika nchi wanachama na kuchochea maendeleo ya kiuchumi, kisiasa na kijamii.

Katika kikao hicho pia walifanya mapitio ya maendeleo yaliyopatikana katika nchi zao, ikiwa ni pamoja na kuimarisha huduma za jamii, kuboresha miundombinu pamoja na kuweka mikakati ya kujenga uchumi stahimilivu na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Masuala mengine yaliyojadiliwa ni pamoja na umuhimu wa kuongeza ajira kwa vijana, kuwawezesha wanawake pamoja na kujenga uchumi jumuishi na stahimilivu kwa maendeleo ya Ukanda wa Kusini mwa Afrika.





 


Top News