Na Victor Masangu,Kibaha

VYAMA Sita Rafiki vya Ukombozi Kusini mwa Afrika vimetakiwa kuendeleza ushirikiano ulioachwa na waasisi wa mataifa hayo ili kuleta maendeleo kwa wananchi.

Hayo yamesemwa kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere (MJNLS) Kwa Mfipa Kibaha na Katibu Mkuu wa Chama cha SWAPO na Mjumbe wa Bodi ya Wadhamini ya Shule hiyo Sophia Shaningwa wakati wa hafla ya Ufunguzi wa Programu hiyo.

Shaningwa amesema kuwa mafunzo hayo yatasaidia wakufunzi hao kuwajengea uwezo viongozi wa vyama hivyo tawala kwani wana nafasi kubwa ya kuleta maendeleo.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bara Aggrey Mwanri ameipongeza shule hiyo kwa kuandaa mafunzo hayo kwa wakufunzi kwani yatasaidia kuleta maendeleo na kukuza uchumi.

Mwanri amesema kuwa huo ni uwekezaji mzuri kwa viongozi ili kupata mbinu mbalimbali ikiwemo za mawsiliano na kuhudumia kwa usawa.

Naye Mkurugenzi wa Masuala ya Kitaaluma na Wanafunzi wa Shule hiyo Profesa Ana Nhampule akielezea kuhusu mafunzo hayo amesema kuwa Shule inavihudumia vyama sita rafiki na kundi pana la viongozi kupitia programu zinazohusiana na vyama, programu maalum kwa ajili ya wizara, taasisi za umma, biashara, na mashirika mengine, pamoja na programu huru kwa viongozi chipukizi na wale waliothibitika.

Nhampule amesema kuwa Mkakati wao unajumuisha uongozi wa vijana EYOLE uongozi wa wanawake kupitia SIWOLEMA, usimamizi wa mashirika ya umma kupitia SLM-PESA na programu za mkakati, utawala, maadili, majadiliano, mawasiliano, mabadiliko ya kiuchumi, maslahi ya taifa, na utendaji wa kitaasisi.

"Katika mzunguko wa Mpango Mkakati wa 2023-2025 MJNLS ilitekeleza programu 93 na kufundisha au kuhitimu washiriki 14,735 inakua kama taasisi ya maarifa ,"amesema Nhampule.

Aidha amesema kuwa ajenda yao ya Utafiti 2025-2035 inaungwa mkono na miundo ya Baraza la Mawazo, Jarida la Uongozi na maktaba inayozidi kukua na ushirikiano wa kieneo wa utafiti.

Vyama hivyo rafiki vinavyoshiriki mafunzo hayo ya siku 45 ni CCM ina 10, ANC tisa, FRELIMO watano , SWAPO watatu, na ZANU-PF 10 ambapo wajumbe wa MPLA hawakuweza kufika kutokana na shughuli za sasa na za dharura za chama chao.




Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara, Ndugu Aggrey Mwanri (MCC), leo Agosti 15, 2026, amekuwa Mgeni Rasmi katika Mkutano wa Hadhara wa Jimbo la Ubungo, ulioandaliwa na Mbunge wa Jimbo hilo, Prof. Kitila Mkumbo, ambaye pia ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji.

Kabla ya kushiriki mkutano huo, Ndugu Mwanri alipokewa katika Ofisi za CCM Mkoa wa Dar es Salaam na Sekretarieti ya CCM Mkoa, chini ya Katibu wa CCM Mkoa, Ndugu Mkandawire.

Aidha, alipokea taarifa fupi kuhusu utendaji wa Chama katika Mkoa huo na kuwashukuru viongozi wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam kwa usimamizi mzuri wa Chama na Serikali.

Akizungumza katika mkutano huo, Ndugu Mwanri amesisitiza umuhimu wa Wabunge, Madiwani pamoja na Wenyeviti wa Serikali za Mitaa kufanya mikutano ya hadhara mara kwa mara ili kuwapa wananchi mrejesho kuhusu utekelezaji wa ahadi zilizotolewa na CCM wakati wa Uchaguzi.

Aidha, amewasihi wananchi kumuunga mkono Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, akieleza kuwa Serikali imeendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika Mkoa wa Dar es Salaam na maeneo mengine nchini.

Kwa upande wake, Prof. Kitila Mkumbo aliwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya CCM mbele ya wananchi wa Jimbo la Ubungo, akieleza hatua zilizochukuliwa katika kuboresha miundombinu, hususan sekta ya barabara.

Prof. Kitila amesema ataendelea kushirikiana na Chama Cha Mapinduzi na Serikali katika kuhakikisha wananchi wa Ubungo wanaendelea kupata huduma na maendeleo yanayostahili.













TAASISI Taasisi ya Safal ALAF Foundation imepokea takriban milioni 20 kupitia safari maalumu maarufu kama The Africa Rally iliyofanyika mwaka huu ambapo washiriki waliendesha kilometa 6000 kutoka Hartbeespoort, Afrika Kusini hadi Bagamoyo, Tanzania, kuchangisha fedha kwa sababu mbalimbali.

Fedha hizo zitatumika kununua vifaa kwa ajili ya Taasisi ya Mafunzo ya Ufundi ya Safal ALAF- The Safal ALAF Technical Training Institute kupitia kampeni maalumu inayojulikana kama ‘Miles for Education’ yenye lengo ya kutoa mafunzo kwa vitendo na kutoa fursa mbalimbali za uwezeshaji kwa vijana. Taasisi hiyo ambayo ni juhudi za ALAF Limited itafungua milango kwa vijana wa kitanzania na kutoa fursa ya mafunzo ya ufundi na mafunzo stadi na kuongeza fursa za kujiajiri au kuajiriwa.

Elimu ni moja ya vipaumbele vya Safal ALAF Foundation kama njia ya kuwezesha vijana. Hii ndio sababu kuu ya ALAF kuwekeza katika taasisi hii iliyoko Arusha sanjari na uwekezaji mwingine katika jamii nchi nzima.

Tukio la mwaka huu lilihusisha washiriki 50 walioendesh amagari ya kizamani na kukatiza katika nchi tano tofauti na baadaye kuhitimisha safari hiyo Bagamoyo.

ALAF Limited’s Head of External Affairs, Ms. Hawa Bayumi, congratulated the pair on their achievement, noting that the initiative supports the development of technical skills and opportunities for young people who will enroll at the facility. “Every mile in this 6,000-kilometre journey represented commitment, resilience, and progress towards impact,” she said.

Bw. Sangeet Shah, ambaye aliiwakilisha ALAF katika tukio hilo pamoja na dereva mwenzake, Tim Pick,ambao waliendesha gari aina ya Mercedez Benz ya zamani, alisema hili kwao lilikuwa tukio la kipekee. “Lengo kuu lilikuwa ni kuchangia katika ujenzi wa Safal ALAF Technical Institute na tunafurahi kuwa tumeweza kukamilisha safari hii kikamilifu na kutimiza malengo kwani taasisi hii itawasaidia vijana wengi kutimiza malengo yao,” alisema Shah.

Alitoa wito kwa wanaopenda kuendelea kuchangia katika mfuko huo kufanya hivyo kupitia www.africarally.com kwani nafasi hiyo bado iko wazi ili kuwezesha ujenzi wa chuo hiki cha ALAF.”Tulipia pale na kujionea mradi huu wa ALAF ambao utawanufaisha watanzania wengi,” aliongeza.

Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano wa ALAF Limited, Bi. Hawa Bayumi aliwapongeza madereva hao na kuongeza kuwa jitihada zao zitasaidia katika kukuza maarifa ya kiufundi na fursa za vijana kujiunga na taasisi hiyo hapo baadaye.

“Kila maili katika safari hii ya km 6000 ilikuwa ni ishara ya kujituma, uthibiti na hatua nzuri katika kupata mafanikio mema, aliongeza.

Naye Bw. Pick alisema tukio hilo limewapa uzoefu mkubwa hasa ikizingatiwa kuwa wameshiriki ili kuchangia fedha za kuwezesha ujenzi wa chuo hicho cha ALAF.

Muandaaji wa tukio hilo maalumu, Bw. Paul Clayton aliwapongeza madereva hao kwa uamuzi wa kushiriki kwa madhumuni ya kuchangisha fedha.

“Zaidi ya Randi milioni 1.1 (Tsh milioni 173) zimekusanywa kupitia tukio hili na zitasaidia katika Nyanja mbalimbali. Chuo cha Ufundi cha ALAF kitapokea takriban Randi 119,000 (Tsh milioni 20) ambazo zinaweza kuongezeka kwani dirisha la kuchangia bado liko wazi kwa mwezi mzima kuanzia sasa,” alisema.

Alishukuru Serikali ya Tanzania kupitia Bodi ya Utalii Tanzania kwa ushirikiano mkubwa walioutoa katika kufanikisha tukio hilo, ambalo lilianzishwa miaka mitano iliyopita, kumalizikia Bagamoyo.

Benki ya NMB imehitimisha ushiriki wake katika Tamasha la Kizimkazi 2026 kwa kuunganisha wananchi na huduma za kifedha pamoja na fursa za kukuza biashara.

NMB ilikuwa miongoni mwa wadhamini wa tamasha hilo lililofikia kilele jana, Agosti 14, Kusini Unguja. Banda la benki hiyo lilitumika kutoa elimu ya fedha na kueleza huduma zinazolenga wafanyabiashara, wajasiriamali na wananchi wa Zanzibar.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, alipotembelea banda hilo, alipokea maelezo kutoka kwa Mkuu wa Idara ya Biashara za Serikali wa NMB, Vicky Bishubo, kuhusu ushiriki wa benki katika tamasha na huduma ilizopeleka kwa wananchi.

Ushiriki huo umeimarisha nafasi ya Kizimkazi kama jukwaa la kutangaza fursa za kiuchumi, kuibua biashara na kuleta huduma muhimu karibu na jamii.

PICHA 1: Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, akisikiliza maelezo kutoka kwa Mwakilishi wa Idara ya Biashara za Serikali wa Benki ya NMB, Vicky Bishubo, alipotembelea banda la benki hiyo katika Tamasha la Kizimkazi 2026, Zanzibar. NMB ilikuwa miongoni mwa wadhamini wa tamasha hilo lililofikia kilele jana.



 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, akikabidhi cheti cha kutambua ushiriki wa NMB katika kufanikisha Tamasha la Kizimkazi 2026 kwa mwakilishi wa benki hiyo.






Na Mwandishi Wetu

UMOJA wa Wahitimu wa Shule ya Sekondari Tosa Maganga (TAO) umeanzisha kampeni ya kuchangisha Sh milioni 250 kwa ajili ya ununuzi wa basi jipya la shule hiyo, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya maadhimisho ya miaka 100 tangu kuanzishwa kwake.

Aidha, imewataka wahitimu wote wa Tosa Maganga na wadau mbalimbali kushirikiana katika kufanikisha ununuzi wa basi hilo, wakisisitiza kuwa mchango wa kila mmoja ni muhimu katika kutimiza azma hiyo.

Hayo yalisema leo jijini Dar es Salaam na Mwenyekiti wa kamati ndogo ya ununuzi wa basi hilo, Iddy Mwerangi, ambaye ni alumnus wa mwaka 1996–1998, alisema TAO imeamua kubeba jukumu hilo ili kuiwezesha shule kupata usafiri wake wa kudumu na kupunguza gharama zinazotumika kukodi magari kwa shughuli mbalimbali.

Alisema basi hilo linalotarajiwa kununuliwa ni aina ya Yutong D14, ambalo litakuwa na uwezo wa kubeba abiria 77, litatumika katika safari za kitaaluma, michezo, shughuli za kijamii pamoja na dharura, huku akieleza kuwa ununuzi wa basi hilo utasaidia kuongeza hadhi ya shule ambayo kwa sasa ni miongoni mwa shule za vipaji maalum.

"TAO tayari imefanya mawasiliano na kampuni ya Yutong nchini China pamoja na wakala wake nchini Tanzania kwa ajili ya kupata maelezo na mahitaji muhimu ya basi hilo,"alisema Mwenyekiti Mwerangi

Kwa mujibu wa Mwerangi, TAO inatarajia kupata fedha hizo kupitia michango kutoka kwa wahitimu wa shule hiyo waliopo ndani na nje ya Tanzania, taasisi, kampuni, wafanyabiashara na watanzania wengine wenye nia ya kuiunga mkono Tosa Maganga.

"Michango yote itapokelewa kupitia akaunti rasmi ya Tosa Maganga Alumni Organization na itaorodheshwa kwa ajili ya kuhakikisha uwazi na uwajibikaji.Kampeni hiyo ni sehemu ya miradi iliyopangwa katika maadhimisho ya miaka 100 ya Tosa Maganga, ambayo yanatarajiwa kufanyika Oktoba 8 hadi 10, 2026, Iringa,"alisema

Alibainisha kuwa kamati ya shule na bodi wameainisha miradi minne, ikiwemo ununuzi wa viti na meza za bwalo la chakula, ukarabati wa mabweni ya Muungano na Madera, pamoja na ununuzi wa basi hilo, TAO imechukua jukumu la kutafuta Sh milioni 250 kwa ajili ya basi, sawa na asilimia 25 ya lengo la jumla la Sh bilioni moja la miradi ya jubilee.

Kwa upande wake, Katibu wa kamati hiyo, Grayon Nyamoga amewataka wahitimu wa shule hiyo kushirikiana katika kuchangisha fedha hizo zitakazotumika kununua basi jipya la shule hiyo.

"Lengo hili linawezekana kutokana na idadi kubwa ya wahitimu waliopo, endapo wahitimu 10,500 watatoa kiwango cha chini cha Sh 50,000 kila mmoja, zaidi ya Sh milioni 500 zinaweza kupatikana, hivyo kuwezesha ununuzi wa basi pamoja na kushiriki katika miradi mingine ya maadhimisho ya miaka 100 ya shule hiyo,"alisema.

Nyamoga alisema TAO imeweka utaratibu wa kuhakikisha fedha zitakazochangwa kwa ajili ya basi zinakuwa salama na zinatumika kwa uwazi, akiwahakikishia alumni kuwa akaunti inayotumika kukusanya michango ni ya taasisi inayotambulika na kusajiliwa.

"Kamati pia imekubaliana kutoa taarifa za makusanyo kwa makundi mbalimbali ya alumni ili kila mhitimu aweze kufuatilia maendeleo ya zoezi hilo na kuwa na imani na matumizi ya fedha zinazokusanywa,"alisema

Aidha, alisema kamati itaendelea kushirikiana na uongozi wa shule, Manispaa pamoja na taasisi na mamlaka husika kuhakikisha mchakato wa ununuzi wa basi unafanyika kwa kuzingatia taratibu zote.
Mwenyekiti wa Kamati Ndogo ya Ununuzi wa Basi la Shule la Tosa Maganga, Iddy Mwerangi
Katibu wa kamati Ndogo ya ununuzi wa basi la shule ya Tosa Maganga, Dk Greyson Nyamoga




Na Oscar Assenga, Kilindi


MKURUGENZI Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Crispian Chalamila amemuahidi Rais Samia Suluhu Hassan kuwa taasisi hiyo itaendelea kufanya kazi kwa bidii na weledi katika kuhakikisha vita dhidi ya rushwa nchini vinafanikiwa.

Chalamila alisema hayo wakati akizindua jengo jipya la ofisi ya TAKUKURU Wilaya ya Kilindi, mkoani Tanga, akisema Serikali imeendelea kuiwezesha taasisi hiyo kwa rasilimali watu, fedha na vitendea kazi ili kuimarisha mapambano dhidi ya rushwa.


Alisema uwekezaji huo ni ishara ya dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt.Samia Suluhu katika kuhakikisha TAKUKURU inakuwa na uwezo wa kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.

“Kwa niaba ya menejimenti ya TAKUKURU, nitoe shukrani za dhati kwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuiwezesha taasisi hii kwa rasilimali watu, vitendea kazi na fedha,” alisema.

Chalamila alisema uwezeshaji huo umewezesha taasisi kujenga ofisi katika mikoa na wilaya mbalimbali, jambo linalowapa watumishi mazingira bora ya kufanyia kazi na wananchi kupata huduma kwa mazingira rafiki.

Ofisi 93 kufikia 2027

Chalamila alisema TAKUKURU imeweka mkakati wa kutenga bajeti kila mwaka kwa ajili ya ujenzi wa ofisi zake, huku akieleza kuwa taasisi hiyo ina ofisi 145 katika mikoa yote 26, wilaya 111 na vituo maalumu sita.


Alisema kati ya ofisi hizo, majengo 70 yanamilikiwa na TAKUKURU na yanapatikana katika mikoa 23, wilaya 46 na kituo maalumu kimoja.

“Majengo yanayoendelea kujengwa katika mwaka wa fedha 2025/2026 na 2026/2027 ni 23, ambayo yanajumuisha ofisi tatu za mikoa na ofisi 20 za wilaya,” alisema.


Alisema kukamilika kwa miradi hiyo kutafanya hadi mwaka 2027 TAKUKURU kuwa na majengo 93 yanayomilikiwa na taasisi hiyo.

Hata hivyo, alisema bado kuna ofisi 52 ambazo hazijafikiwa na mpango huo wa ujenzi, zikiwa katika mikoa miwili, wilaya 45 na vituo maalumu vitano.

Kwa upande wa jengo la TAKUKURU Kilindi, Chalamila alisema limegharimu Sh450.7 milioni hadi kukamilika, ikiwa ni ongezeko la Sh3.1 milioni, sawa na asilimia 0.7 ya bajeti ya awali.

Alisema ongezeko hilo lilitokana na changamoto mbalimbali zilizojitokeza wakati wa utekelezaji wa mradi.

Aliwapongeza wataalamu wa TAKUKURU, Mkoa wa Tanga na Wilaya ya Kilindi kwa kuhakikisha ujenzi wa jengo hilo unakamilika kwa wakati.

Pia aliwataka watumishi wa TAKUKURU katika wilaya ya Kilindi na maeneo mengine yenye majengo mapya kuyatunza pamoja na vitendea kazi walivyopewa ili yaweze kutumika kwa muda mrefu.

“Serikali imewawezesha kwa kiwango kikubwa. Hilo ni deni ambalo tunapaswa kulilipa kwa kufanya kazi kwa bidii na weledi zaidi ili dhamira ya Serikali ya kuitokomeza rushwa nchini itimie,” alisema.
DC aomba jenereta

Mkuu wa Wilaya ya Kilindi, Hashim Mgandilwa, aliishukuru Serikali kwa kuendelea kuziwezesha taasisi zake kuwa na miundombinu bora inayorahisisha utoaji wa huduma kwa wananchi.


Mgandilwa alisema ujenzi wa jengo hilo ni hatua muhimu kwa wilaya hiyo, ambayo tangu kuanzishwa kwake mwaka 2002 imekuwa ikikabiliwa na changamoto ya upungufu wa miundombinu ya ofisi.

Hata hivyo, aliomba TAKUKURU kuangalia uwezekano wa kuiwezesha ofisi hiyo kupata jenereta kutokana na changamoto ya kukatika kwa umeme katika eneo hilo.


“Jengo ni zuri, lakini haitakuwa na maana kama mwananchi akija kupata huduma anaambiwa umeme umekatika. Tunaomba muone namna ya kupata jenereta ili huduma ziendelee muda wote,” alisema.

Alisema Serikali tayari imeweka mpango wa kuimarisha umeme katika eneo hilo na imetenga Sh98 milioni kwa ajili ya ujenzi wa kituo kidogo cha kupoza umeme.

TAKUKURU Kilindi yapata ofisi baada ya miaka 20

Kwa upande wake, Kamanda wa TAKUKURU Mkoa wa Tanga, Ramadhan Ndwatah, alisema kabla ya kupata jengo hilo, taasisi hiyo ilifanya kazi katika majengo ya kupanga kwa takribani miaka 20.


Alisema kuanzia mwaka 2005 hadi 2010 walikuwa katika majengo ya kupanga Kata ya Songe, kabla ya kuhamia Kata ya Bokwa, Kijiji cha Legeza Mwendo, ambako walikaa hadi mwaka 2026.


Ndwatah alisema hali hiyo ilisababisha changamoto mbalimbali, ikiwamo majengo kutokidhi mahitaji ya kisasa ya ofisi, changamoto za mawasiliano na ulazima wa kufanya ukarabati mara kwa mara.

Alisema pia kuwepo kwa ofisi katika majengo ya makazi ya watu kulikuwa kunawafanya baadhi ya wananchi kukosa uhuru wa kufika kutoa taarifa za vitendo vya rushwa kwa utulivu.


“Tunamshukuru Mkurugenzi Mkuu kwa uamuzi wa kutujengea jengo hili la kisasa. Litasaidia wananchi wa Kilindi kufika kwa uhuru na kupata huduma katika mazingira bora,” alisema.


Jengo hilo jipya linatarajiwa kuongeza ufanisi wa TAKUKURU Wilaya ya Kilindi katika kutekeleza majukumu yake, ikiwamo kupokea taarifa na malalamiko ya wananchi kuhusu vitendo vya rushwa.

Taasisi ya Elimu Tanzania (TET) inashiriki katika Maadhimisho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu 2026, yanayofanyika katika viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara, mkoani Tanga.

Maadhimisho hayo yameanza leo, Agosti 15, 2026, na yanatarajiwa kuhitimishwa Agosti 24, 2026, yakibeba kaulimbiu isemayo: “Elimu, Ujuzi na Ubunifu, Njia ya Kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.”

Katika maadhimisho hayo, wadau mbalimbali wa sekta ya elimu, ujuzi, sayansi, teknolojia na ubunifu wameendelea kujitokeza kushiriki na kuonesha mchango wao katika maendeleo ya taifa.

Miongoni mwa viongozi walioshiriki ni Mkurugenzi wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Ladslaus Mnyone.

Maadhimisho hayo yamewakutanisha zaidi ya taasisi 100 kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, zikiwa na lengo la kuonesha bunifu, ujuzi na fursa mbalimbali zinazoweza kuchangia katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.




Vodacom Tanzania kupitia Vodacom Tanzania Foundation inaendelea kuchangia uboreshaji wa mazingira ya kujifunzia kwa watoto kupitia ukarabati na ujenzi wa madarasa katika shule tatu za msingi za umma zilizopo Pwani, Ruvuma na Morogoro.

Mpango huu, unaotekelezwa kwa kuzingatia mahitaji yaliyobainika, unalenga zaidi kusaidia watoto wenye mahitaji maalum katika shule za umma. Kupitia mpango huu, madarasa sita yamefanyiwa maboresho, ambapo shule za msingi Vikindu - Mkuranga, Mahilo - Songea na Ihowanja - Morogoro zimepatiwa madarasa mawili kila shule.. Kati ya madarasa hayo, mawili yamekarabatiwa na manne yamejengwa upya. Maboresho haya yanatarajiwa kuwafikia wanafunzi 4,838, wakiwemo 117 wenye mahitaji maalum, pamoja na walimu 52, sambamba na utoaji wa madawati 90 kwa shule zote tatu.

Hafla ya kwanza ya makabidhiano hayo ilifanyika katika Shule ya Msingi Vikindu, Wilaya ya Mkuranga, ambapo Vodacom Tanzania ilikabidhi madarasa pamoja na madawati hayo. Mpango huo utaendelea katika Shule ya Msingi Mahilo mkoani Ruvuma, tarehe 20 Agosti 2026 na Shule ya Msingi Ihowanja, Morogoro, tarehe 27 Agosti 2026.

Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano katika Shule ya Msingi Vikindu, George Nyanda, Meneja Mauzo Kanda ya Dar es Salaam na Pwani wa kampuni ya Vodacom Tanzania alisema, “katika Shule ya Msingi Vikindu, madarasa haya mawili yanalenga kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa watoto na kufundishia kwa walimu. Kuitikia mahitaji ya jamii kunahitaji kuelewa mambo yanayoweza kuleta tofauti katika maisha ya kila siku ya watoto, hususan wale wenye mahitaji maalum. Tunafurahi kuchangia katika kuweka mazingira ambayo yatawawezesha wanafunzi kujifunza kwa utulivu na kujisikia kuwa sehemu ya jamii ya shule.”

Akizungumzia msaada huo katika Shule ya Msingi Ihowanja, Chiha Nchimbi, Mkuu wa Kanda ya Kati wa kampuni hiyo aliongeza, “katika Shule ya Msingi Ihowanja, madarasa haya mawili mapya yanaongeza nafasi muhimu za kujifunzia kwa jamii ya shule. Haya ni maeneo ambayo yatatumika kila siku kwa ajili ya masomo, kukuza ujuzi na kuwawezesha watoto kuendelea kujifunza na kukua. Haya ndiyo mahitaji ya jamii ambayo Vodacom Tanzania Foundation inalenga kuyaitikia kupitia mipango yake.”

Kuhusu namna msaada huo utakavyoleta neema katika Shule ya Msingi Mahilo, Mkuu wa Kanda ya Nyanda za Juu Kusini wa Vodacom Tanzania, Abednego Mhagama alifafanua, “katika Shule ya Msingi Mahilo, madarasa haya mawili mapya yatawapatia wanafunzi na walimu mazingira bora zaidi ya kujifunzia na kufundishia. Darasa si jengo pekee; ni sehemu ambayo watoto hutumia muda wao mwingi kujifunza na kujiandaa kwa maisha yao ya baadaye. Tunafurahi kuchangia katika kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa jamii hii.”

Maboresho haya ya madarasa ni sehemu ya mchango unaoendelea wa Vodacom Tanzania Foundation katika kusaidia elimu na kuboresha mazingira ya kujifunzia katika jamii mbalimbali nchini, kwa kuzingatia mahitaji yaliyobainika. Foundation imewahi kusaidia mipango kama hii hapo awali na inaendelea kuelekeza juhudi zake katika maeneo yenye mahitaji.
Mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya ya Mkuranga Helen Kulwa Benjamini (kushoto) akishikana mkono na Meneja Mauzo Mwandamizi wa Kanda ya Dar es salaam na Pwani wa Kampuni ya Vodacom Tanzania Plc George Nyanda (kulia) wakati wa makabidhiano ya madarasa mawili yaliyoboreshwa pamoja na madawati 30 katika shule ya msingi Vikindu chini ya mpango wa kampuni hiyo wa kurejesha kwa jamii yaliyofanyika kwa lengo la kuwajengea wanafunzi wa shule ya msingi mazingira bora ya kujifunzia. Hafla hiyo limefanyika tarehe 14 Agosti 2026, Vikindu, Mkoani Pwani.
Mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya ya Mkuranga Madam Helen Kulwa Benjamini (kulia) akishikana mkono na Meneja Mauzo Mwandamizi wa Kanda ya Dar es salaam na Pwani wa Kampuni ya Vodacom Tanzania Plc George Nyanda (kushoto) wakati wa makabidhiano ya madarasa mawili yaliyorekebishwa pamoja na madawati 30 yaliyotolewa na Kampuni hiyo. Tukio hilo lilishuhudiwa Mwenyekiti wa Kijiji cha Vikindu Said Nguvumari (kulia) na Mwenyekiti wa CCM kata ya Vikindu Bahati Ali Mawinga.
Wafanyakazi wa Kampuni ya Vodacom Tanzania PLC wakiwa kwenye picha ya pamoja kwenye moja ya darasa lililofanyiwa marekebisho katika shule ya msingi vikindu.
Moja ya darasa lililofanyiwa marekebisho na Kampuni ya Vodacom Tanzania PLC katika shule ya msingi Vikindu.




DAR ES SALAAM: Usiku wa Tamasha la Imbeju Sauti Moja, lililoandaliwa na CRDB Foundation, umeacha gumzo kubwa kwa mashabiki wa burudani baada ya nyota wa muziki kutoka Marekani, Trey Songz, kuamua kumualika staa wa Tanzania, Diamond Platnumz, jukwaani.

Tamasha hilo lililofanyika katika viwanja vya Posta, Kijitonyama jijini Dar es Salaam, liliwakutanisha mashabiki wa muziki waliojitokeza kwa wingi kushuhudia burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali wa ndani na nje ya Tanzania.

Hata hivyo, ujio wa Trey Songz ulikuwa miongoni mwa matukio yaliyotikisa zaidi usiku huo. Msanii huyo aliwasha jukwaa kwa vibao vyake maarufu kabla ya kumshangaza umati kwa kumkaribisha Diamond Platnumz.

Mara tu Diamond alipotokea jukwaani, shangwe na mayowe vilitawala eneo hilo, huku mashabiki wakifurahia kuwaona mastaa hao wawili wakishirikiana mbele yao.

Kilele cha burudani hiyo kilikuwa pale Trey Songz na Diamond Platnumz walipotumbuiza kwa pamoja wimbo wao mpya, ambao uliwasilishwa mbele ya mashabiki kwa mara ya kwanza kwenye jukwaa hilo.

Ushirikiano huo uliifanya Imbeju Sauti Moja kuwa moja ya matukio yaliyovuta hisia kubwa katika usiku huo, huku mashabiki wakipata nafasi ya kushuhudia kwa mara ya kwanza namna mastaa hao walivyounganisha ladha ya muziki wa Tanzania na R&B ya Marekani.

Mbali na Trey Songz na Diamond Platnumz, tamasha hilo lilinogeshwa na burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali wa Tanzania na nje ya nchi, jambo lililofanya usiku huo kuwa wa muziki, dansi na burudani kwa mashabiki waliohudhuria.

Kwa kifupi, Trey Songz kumuita Diamond Platnumz jukwaani na kutumbuiza pamoja kulikuwa moja ya matukio yaliyoacha alama kubwa katika Tamasha la Imbeju Sauti Moja.

Mkurugenzi wa CRDB Bank, Dkt. Abdulmajid Nsekela (wa pili kulia), akiburudika pamoja na baadhi ya wageni wake wakati wa Tamasha la Imbeju Sauti Moja, lililoandaliwa na CRDB Foundation katika viwanja vya Posta, Kijitonyama, Dar es Salaam. Usiku huo uliambatana na burudani ya nguvu kutoka kwa wasanii mbalimbali wa ndani na nje ya Tanzania, huku wageni wakijumuika kufurahia muziki na shamrashamra za tamasha hilo.




















 














Top News