Na Mwandishi wetu, Babati


Mkoa wa Manyara umeweka mkakati wa kuhakikisha watoto 670,000 wenye umri chini ya miaka 10 wanafikiwa na kupata chanjo katika Kampeni ya Chanjo ya Polio ya Matone, huku maandalizi ya Uzinduzi wa Kitaifa wa Kampeni hiyoyakiendelea kufanyika mkoani humo.

Akizungumza baada ya kupata nafasi ya kuonana na Kaimu Meneja Mpango wa Taifa wa Chanjo Dkt Georgina Joachim kutoka Wizara ya Afya pamoja na Dkt Floriani Tinuga kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI, Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Cuthbert Sendiga, amesema mkoa uko tayari kutekeleza zoezi hilo kwa ufanisi.

Mhe. Sendiga amesisitiza kuwa Serikali ya Mkoa imejipanga kuhakikisha hakuna mtoto atakayeachwa nyuma, na kwamba juhudi zote zitaelekezwa katika kuwafikia watoto wote 670,000 wanaolengwa kupata chanjo kuanzia tarehe 27 hadi 30 Agosti 2026.

Amesema ushirikiano kati ya Serikali, wataalamu wa afya, viongozi wa maeneo, wazazi, walezi na jamii kwa ujumla ni muhimu katika kuhakikisha kampeni hiyo inafikia malengo yaliyowekwa.

Kampeni hiyo inalenga kuimarisha kinga dhidi ya ugonjwa wa Polio kwa watoto na kuongeza uelewa wa jamii kuhusu umuhimu wa kuwapeleka watoto kupata chanjo kwa wakati.

Katika utekelezaji wa kampeni, timu za wataalamu wa afya zinatarajiwa kushirikiana na viongozi na jamii watapita nyumba kwa nyumba, mashuleni, kwenye minada, masoko, nyumba za Ibada na maendeo yenye mikusanyiko kuwatafuta na kuwapatia chajo walengwa wote wa zoezi hili.

Mkoa wa Manyara pia unaendelea na maandalizi kuelekea uzinduzi wa kampeni ya chanjo ya Polio ya Matone Kitaifa tarehe 27 Agosti 2026, huku uongozi wa Mkoa ukisisitiza utayari wake wa kuhakikisha zoezi hilo linafanyika kwa mafanikio.

 
Mkuu wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere (MNMA) Profesa Haruni Mapesa akisaini Kitabu wakati alipotembelea Banda la TIA katika Wiki ya Elimu Kitaifa ,Ujuzi na Ubunifu inayoendelea katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara,Jijini Tanga.
Mkuu wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere (MNMA) Profesa Haruni Mapesa akipata maelezo kutoka Mkuu wa Sehemu - Ukuzaji na Uendelezaji wa wanafunzi kitaaluma na kitaalam wa TIA Imani  Matonya  kuhusiana na bunifu mbalimbali wa wanafunzi na wahitimu was TIA  walizoleta katika Maonesho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu ,Ujuzi na Ubunifu  Kwakati Mkuu wa Chuo hicho  alipotembelea Banda la TIA katika Wiki ya Elimu Kitaifa ,Ujuzi na Ubunifu inayoendelea katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara,Jijini Tanga.
Baadhi ya Wahitimu na Wanafunzi wa TIA  ambao wenye bunifu ambazo zimesimamiwa TIA kwenye maonesho ya Wiki ya Elimu Kitaifa ,Ujuzi na Ubunifu inayoendelea katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara,Jijini Tanga.



Na Mwandishi Wetu
SERIKALI imetakiwa kuongeza uwekezaji katika tafiti na ubunifu unaofanywa na vyuo vya elimu ya juu nchini ili kusaidia kutatua changamoto mbalimbali za jamii na kuongeza mapato ya taifa kupitia teknolojia zinazozalishwa na wataalamu wazawa.
 
Wito huo umetolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo Husna Sekiboko, wakati alipotembelea Banda la Chuo Kikuu  Dodoma (UDOM) katika Maonesho ya Wiki ya Elimu Kitaifa, Ujuzi na Ubunifu yanayoendelea katika Viwanja vya Usagara, Tanga.
 
Sekiboko amesema tafiti na ubunifu unaofanywa na vyuo vya elimu ya juu nchini umefikia hatua kubwa na una uwezo wa kutatua changamoto mbalimbali zinazolikabili taifa, hivyo unapaswa kupewa kipaumbele, bajeti na uwezeshaji wa kutosha. Amesema miongoni mwa teknolojia iliyomvutia ni mfumo wa ultrasound uliobuniwa na wataalamu wa UDOM, unaolenga kutoa huduma za uchunguzi wa afya kwa gharama nafuu ikilinganishwa na baadhi ya vifaa vinavyopatikana sokoni. Kwa mujibu wa Sekiboko, teknolojia hiyo inaweza kusaidia kufuatilia maendeleo ya mtoto akiwa tumboni kuanzia wiki 12 za ujauzito, pamoja na kusaidia katika uchunguzi wa afya ya mama na mtoto.
 
Amesema ubunifu huo ni mfano wa teknolojia zinazopaswa kuendelezwa na kusambazwa katika vituo vya afya nchini kabla ya Tanzania kuanza kuzisafirisha katika nchi nyingine za Afrika.
 
“Tunatakiwa kuwekeza na kuendeleza ufumbuzi ambao umefanyika kwa teknolojia hii iweze kukua, lakini isambae na iweze kutumika kwenye vituo vya afya nchi nzima. Baadaye tuuze kwenye nchi za jirani,” amesema.
 
Amesema Tanzania kwa sasa inatumia teknolojia kutoka nchi mbalimbali, zikiwamo China na India, katika sekta za afya, kilimo na maeneo mengine, hivyo ni wakati muafaka kwa taifa kuanza kuzalisha na kuuza teknolojia zinazobuniwa na wataalamu wa ndani. Sekiboko amesema teknolojia ya ultrasound iliyobuniwa UDOM inaweza kuwa miongoni mwa bidhaa za “Made in Tanzania” zinazoweza kutumika ndani ya nchi na kuuzwa nje, hatua ambayo inaweza kuongeza mapato ya vyuo na taifa, pamoja na kutoa ajira kwa wataalamu watakaohusika katika uzalishaji na matumizi yake.
 
Amesema ubunifu unaofanywa na vyuo unahitaji bajeti, uwezeshaji na kuunganishwa na masoko ili bidhaa na teknolojia zinazozalishwa ziweze kutumika katika taasisi mbalimbali za Serikali. Ameshauri Serikali kuingia mikataba na vyuo vya ndani kwa ajili ya kupata bidhaa na teknolojia zinazohitajika badala ya kutegemea zaidi bidhaa kutoka nje.
 
“Serikali ichukue sasa vile ambavyo vinazalishwa kwenye vyuo, iwe ndio outsource yao, badala ya kwenda kununua mashine nyingine au kuingia mikataba na China na kwingineko, waingie mikataba na vyuo,” amesema Sekiboko. Amesema hatua hiyo itasaidia kuimarisha uwezo wa vyuo, kukuza tafiti na kuhakikisha wataalamu waliobuni teknolojia hizo wanapatikana kwa urahisi wakati wa matengenezo au kutatua changamoto zinazoweza kujitokeza.
 
Katika hatua nyingine, Sekiboko ametoa wito kwa wananchi wa Tanga na mikoa jirani, ikiwamo Pwani, Dar es Salaam, Morogoro, Kilimanjaro, Arusha na Manyara, kujitokeza kwa wingi kutembelea Maonesho ya Wiki ya Elimu Kitaifa, Ujuzi na Ubunifu yanayofanyika Usagara.
 
Amesema maonesho hayo ni ya kitaifa na yameshirikisha vyuo na taasisi mbalimbali kutoka maeneo tofauti ya Tanzania, hivyo wananchi wana fursa ya kujifunza kuhusu elimu, ujuzi, tafiti na ubunifu unaofanywa nchini. Amesema wananchi wenye mahitaji ya elimu ya juu, wanaotarajia kuwapeleka watoto wao vyuoni au wanaotaka kujifunza kuhusu fursa za ujuzi na teknolojia wanapaswa kutumia nafasi hiyo kutembelea mabanda yaliyopo katika maonesho hayo.
 
“Ni jambo la ajabu sana tukifunga haya maonyesho, bado kuna Watanga huko nyumbani hajaja kuji, kushughulikia nini kinaendelea hapa. Wajitokeze, waje watembelee haya mabanda,” amesema.
 
Amesema ushiriki wa wananchi utasaidia kuongeza uelewa kuhusu kazi zinazofanywa na wasomi, wataalamu na wabunifu nchini, pamoja na namna teknolojia hizo zinavyoweza kutumika kutatua changamoto mbalimbali katika jamii.
 
Amesisitiza kuwa wananchi wote wanapaswa kutumia fursa hiyo kufika Usagara na kujionea ubunifu na teknolojia mbalimbali zinazoonyeshwa katika maonesho hayo.







Na Mwandishi Wetu
MKUU wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere (MNMA) Profesa Haruni Mapesa, amesema maonyesho ya elimu, ujuzi na ubunifu ni jukwaa muhimu kwa taasisi za elimu kuonyesha kazi zinazofanywa na wanafunzi pamoja na kuwafungulia vijana fursa mbalimbali za kujifunza na kuendeleza vipaji vyao.

Profesa Mapesa ametoa kauli hiyo wakati akizungumza kuhusu ushiriki wa chuo hicho katika maonyesho ya elimu, ujuzi na ubunifu yanayoendelea mkoani Tanga, akimpongeza Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, pamoja na Wizara hiyo kwa kuendelea kusimamia maonyesho hayo na kuwa na mafanikio.

Amesema maonyesho hayo yamekuwa na umuhimu kwa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere kwa kuwa yanatoa nafasi ya kuonyesha programu zinazotolewa na chuoni ikiwemo mafunzo yanayohusiana na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), pamoja na kazi za ubunifu zinazofanywa na wanafunzi.

“Tunajivunia kupata fursa ya kuonyesha kazi za vijana wetu, ubunifu wao katika sayansi, teknolojia na maeneo mbalimbali. Ubunifu huu umekuwa na mguso mkubwa na tunaamini siku zijazo utakuwa na matokeo makubwa zaidi,” amesema Profesa Mapesa.

Amesema chuo kina mpango wa kuendeleza ubunifu wa wanafunzi kwa kuunganisha kazi hizo na watumiaji na wadau wakubwa ili zitumike zaidi katika shughuli za uzalishaji na kuchangia maendeleo ya uchumi.

Profesa Mapesa amesema maonyesho hayo pia yamekuwa fursa kwa vijana wanaotaka kujiunga na Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere kupata taarifa kuhusu programu mbalimbali zinazotolewa na chuo hicho, huku baadhi yao wakipata huduma za usajili na maelekezo ya kujiunga na programu hizo moja kwa moja katika banda la chuo.

Ameeleza kuwa chuo kinatoa programu za umahiri, shahada ya kwanza, pamoja na diploma, huku akiwataka wananchi wa Tanga kutembelea maonyesho hayo, hususan banda la Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, ili kupata fursa ya kujifunza zaidi kuhusu huduma na programu zinazotolewa na taasisi hiyo.

Aidha, amesema chuo hicho kina nafasi ya kipekee katika kuhifadhi na kutangaza historia ya Muasisi wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, kupitia machapisho, kumbukumbu na hotuba zake ambazo, amesema, zimekuwa na mchango mkubwa katika historia ya Tanzania na Afrika.

Profesa Mapesa amewashukuru waandaaji wa maonyesho hayo pamoja na vyombo vya habari kwa kuendelea kuhabarisha umma kuhusu shughuli za maonyesho na kazi zinazofanywa na taasisi za elimu. Pia amemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kusisitiza umuhimu wa elimu, ujuzi na ubunifu katika maendeleo ya taifa.

Amesema uwekezaji unaoendelea katika elimu, ujuzi na ubunifu ni muhimu katika kujenga Taifa lenye vijana wenye uwezo wa kutumia maarifa na teknolojia kutatua changamoto na kuchangia maendeleo ya Tanzania.

 

Na Mwandishi Wetu.

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imewataka Waandishi wa Habari wa Crown Media kulinda imani ya umma kwa kuzingatia weledi, maadili, uadilifu na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao.

Wito huo umetolewa wakati wa mafunzo ya siku mbili yaliyotolewa na JAB kwa Waandishi wa Habari wa Crown Media, kuanzia Agosti 18 hadi 19, 2026, jijini Dar es Salaam yakilenga kuwaongezea maarifa na kuwajengea uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria, maadili na viwango vya taaluma ya uandishi wa habari.

Akiwasilisha Mada kuhusu Msingi na Mfumo wa Kisheria unaosimamia Sekta ya Habari nchini Tanzania katika mafunzo hayo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, amewasihi Waandishi wa Habari kuthamini na kulinda taaluma yao kwa kuzingatia misingi inayowaongoza katika utekelezaji wa majukumu yao.

“Waandishi wa Habari tunapaswa kuthamini na kulinda taaluma yetu wenyewe. Weledi, maadili na uadilifu ndiyo msingi wa kuaminika kwa mwandishi na sekta ya habari kwa ujumla,” amesema Wakili Kipangula. 

Kwa upande wake, Dkt. Egbert Mkoko amewataka Waandishi wa Habari kuzingatia maadili katika kila hatua ya kazi zao, akieleza kuwa maadili ndiyo msingi wa uandishi wa habari unaowajibika na wenye tija kwa jamii.

“Mwandishi wa Habari anapaswa kuzingatia maadili ya kazi katika kila hatua ya utekelezaji wa majukumu yake, kwa kuwa uadilifu na uwajibikaji ndiyo msingi wa taaluma hii,” amesema Dkt. Mkoko alipokuwa akifafanua mada Kuhusu Maadili ya Utangazaji na makosa ya kimaadili yanayofanywa mara kwa mara.

Naye Mjumbe wa JAB na Kaimu Meneja wa Huduma za Kiswahili wa Shirika la Magazeti ya Serikali (TSN), Bw. Mgaya Kingoba, akiwasilisha mada kuhusu uzalendo, amewataka Waandishi wa Habari kutumia taarifa kwa usahihi na kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia maslahi ya umma.


 Wakizungumza wakati wa tathmini ya mafunzo hayo, baadhi ya Waandishi wa Habari wa Crown Media wamesema wamepata uelewa mpana kuhusu Sheria ya Huduma za Habari, hali iliyowasaidia kuondokana na fikra potofu zilizotokana na tafsiri zisizo sahihi zinazotolewa katika jamii kuhusu Sheria hiyo. Pia wameomba mafunzo kama hayo kutolewa mara kwa mara ili kuwajengea uwezo Waandishi wa Habari.

“Kwa kweli, changamoto tuliyonayo katika vyombo vyetu vya habari ni kushindwa kutofautisha maoni binafsi na uchambuzi wa kitaaluma, pamoja na kushindwa kutenganisha nafasi ya mtu binafsi na wajibu wake kama mwanataaluma. Pia kumekuwa na dhana kwamba Bodi ipo kwa ajili ya kuwadhibiti Waandishi wa Habari, pamoja na uelewa mdogo kuhusu ithibati, umuhimu wake na nafasi yake katika kulinda heshima ya taaluma,” amesema Imani Luvanga mmoja wa washiriki.

Mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa majukumu ya JAB kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, yanayolenga kuimarisha weledi, uadilifu, uwajibikaji na tija katika taaluma ya uandishi wa habari.




Na Avila Kakingo
CHUO Kikuu cha Aga Khan kupitia Taasisi ya Maendeleo ya Elimu Afrika Mashariki (IED, EA), kimewakutanisha waelimishaji wa walimu, watunga sera, watafiti, viongozi wa shule, washirika wa maendeleo, walimu wanafunzi na wataalamu wa elimu kutoka Afrika Mashariki na maeneo mengine kujadili mustakabali wa uandaaji wa walimu.

Mkutano huo wenye kaulimbiu “Kufikiria Upya Uandaaji wa Walimu: Mabadilishano ya Kujifunza Afrika Mashariki kuhusu Ubunifu na Utendaji”, unalenga kutoa jukwaa la kubadilishana uzoefu, kuchunguza mbinu bunifu na kuandaa kwa pamoja suluhisho la kuimarisha uandaaji wa walimu. Akizungumza katika mkutano huo, Mkuu wa IED, EA, Profesa Jane Rarieya, amesema mustakabali wa elimu katika Afrika Mashariki hautegemei kuwa na walimu wa kutosha pekee, bali namna wanavyoandaliwa, kusaidiwa na kuwezeshwa katika taaluma zao.

Profesa Rarieya amesema mabadiliko ya elimu yanachochewa na matumizi ya teknolojia za kidijitali na akili bandia (AI), mabadiliko ya tabianchi, ongezeko la utofauti na ujumuishi pamoja na mabadiliko ya matarajio kuhusu elimu. Amesema mkutano huo unatoa fursa kwa wadau kujifunza kutoka kwa kila mmoja, kuimarisha ushirikiano kati ya shule, vyuo vikuu, jamii na mifumo ya elimu, na kutafakari upya namna ya kuwaandaa walimu kukabiliana na mahitaji ya madarasa ya sasa.

Mabadilishano hayo yanafanyika kwa mtazamo wa kujifunza kwa vitendo na kushirikishana uzoefu, kupitia vikao vya kubadilishana uzoefu, maabara za utekelezaji, madarasa maalumu, mijadala ya pande zote na majadiliano ya paneli. Kupitia vikao hivyo, washiriki wanajadili changamoto zinazofanana, kujifunza kutokana na mazingira mbalimbali na kujenga ushirikiano wa kuimarisha mifumo ya elimu katika ukanda huo.

Eneo jingine linalopewa kipaumbele ni kuwawezesha walimu kuwa na uwezo na uhuru wa kitaaluma wa kushiriki katika mageuzi ya elimu. IED, EA imeeleza kuwa kadri nchi zinavyoendelea kutumia mitaala inayozingatia umahiri, walimu wanahitaji kuwa na uwezo wa kuelewa mahitaji ya wanafunzi, kufanya maamuzi sahihi ya kitaaluma, kutathmini ujifunzaji, kubadilisha mbinu za ufundishaji na kushirikiana na jamii wanazozihudumia.

Kwa mujibu wa IED, EA, mabadilishano hayo ni wito kwa walimu, serikali, vyuo vikuu, shule, jamii na washirika wa maendeleo kushirikiana katika kufikiria upya uandaaji wa walimu Afrika Mashariki. Hatua zinazopendekezwa ni pamoja na kuimarisha mafunzo ya vitendo na ulezi kwa walimu wanafunzi, kujenga jumuiya za kujifunza kitaaluma kwa walimu wanaoanza kazi na kuwapa walimu wenye uzoefu nafasi ya kuwa viongozi, walezi na washiriki katika ubunifu na tafiti za elimu.
Kwa upande wake, Mhadhiri wa Taasisi hiyo, Dkt. Nipael Mrutu, amesema kongamano hilo linalenga kutafakari aina ya mwalimu anayehitajika katika dunia inayobadilika kwa kasi.

Dkt.Mrutu amesema fursa hiyo inawawezesha wataalamu kubadilishana uzoefu kuhusu mbinu mbalimbali za ufundishaji, kutathmini zilizofanikiwa na ambazo hazikutoa matokeo yaliyotarajiwa na kutafuta njia bora za kuboresha elimu.

Amesema ubunifu ni muhimu kwa mwalimu wa sasa kwa kuwa anapaswa kutumia mbinu zinazowawezesha wanafunzi kujifunza kwa ufanisi na kukabiliana na mahitaji yanayobadilika katika jamii na dunia.

Naye mwalimu wa Shule ya Sekondari Jangwani na kiongozi wa Chama cha Walimu wa Somo la Kiingereza Tanzania, Ayub Msuya, amesema walimu wanapaswa kubadilisha mtazamo wa kuwalaumu wanafunzi wanaposhindwa kuelewa na badala yake kutafuta mbinu mpya zinazolingana na mahitaji yao.

Msuya amesema walimu wa Afrika Mashariki wanapaswa kujifunza kutoka kwa wenzao na kubadilishana mbinu za ufundishaji, ikiwamo matumizi sahihi ya teknolojia.

Amesema kwa somo la Kiingereza, walimu wanapaswa kuzingatia mazingira ya lugha wanamoishi wanafunzi na kuwajengea uwezo wa kuelewa, kuchambua na kutumia maarifa wanayopata.

Ameongeza kuwa kongamano hilo limefika wakati mwafaka kwa kuwa linawawezesha walimu kujifunza kutoka kwa wenzao wa nchi nyingine za Afrika Mashariki na kupata mbinu zitakazosaidia kuandaa wanafunzi wenye uwezo wa kuwasiliana, kuchambua na kutumia maarifa katika maisha ya sasa na yajayo.

Kwa mujibu wa Taasisi ya Maendeleo ya Elimu Afrika Mashariki, kongamano hilo pia linalenga kuimarisha ushirikiano kati ya walimu, serikali, vyuo vikuu, shule, jamii na washirika wa maendeleo katika kuboresha uandaaji wa walimu katika ukanda huo.

Kupitia mijadala ya vikundi, maabara za utekelezaji, madarasa maalumu, meza za majadiliano na mijadala ya pamoja, washiriki wanajadili namna ya kuimarisha mafunzo ya vitendo na malezi kwa walimu wanafunzi, kujenga jumuiya za kitaaluma kwa walimu wanaoanza kazi na kuwawezesha walimu wenye uzoefu kushiriki katika uongozi, utafiti na ubunifu wa elimu.



Matukio mbalimbali katika picha.
Picha ya pamoja


Na Mwandishi Wetu, Tanga
CHUO cha Kodi (ITA) kimeshiriki Maonesho ya Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanayoendelea katika Viwanja vya Usagara jijini Tanga, kwa kutoa elimu kuhusu majukumu ya Chuo hicho pamoja na fursa za mafunzo zinazotolewa.

Wanafunzi na wadau mbalimbali waliotembelea banda la ITA wamepata fursa ya kufahamu kwa kina kuhusu programu za mafunzo zinazotolewa na Chuo hicho, huku wakihamasishwa kujiunga na mafunzo hayo.

Maonesho hayo yaliyoanza Agosti 15, 2026, yamekuwa pia jukwaa kwa ITA kuwaelimisha wananchi kuhusu nafasi ya taaluma mbalimbali katika Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na maeneo mengine ya ajira.

Akizungumza na wanafunzi waliotembelea banda hilo, Afisa Mkuu wa Uhusiano wa Umma wa ITA, Oliver Njunwa, amesema mwanafunzi anayelenga kufanya kazi TRA anapaswa kuzingatia masomo yote kwa kuwa Mamlaka hiyo inaajiri wataalamu wenye taaluma mbalimbali.

“TRA ina wafanyakazi wenye taaluma mbalimbali, hivyo mwanafunzi anatakiwa kuzingatia masomo yote na kufanya vizuri katika masomo yake,” amesema Njunwa.

Aidha, amewataka wanafunzi wanaotaka kusoma ITA kutokuwa na mtazamo wa kwamba mhitimu wa Chuo hicho anapaswa kufanya kazi TRA pekee, bali kuwa tayari kufanya kazi katika taasisi au maeneo mengine ambako taaluma zao zinahitajika.

“Mwanafunzi aliyesoma ITA anajengwa kufanya kazi sehemu yoyote ambayo taaluma aliyoisomea inahitajika pamoja na kujiajiri,” amesema.

Maonesho ya Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanaendelea katika Viwanja vya Usagara jijini Tanga hadi Agosti 24, 2026.

Dar es Salaam.
MFUKO wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) umeendesha mafunzo maalum kwa waandishi wa habari kuhusu masuala ya hifadhi ya jamii, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuongeza uelewa wa umma na wanachama kuhusu huduma, haki na wajibu unaotolewa na Mfuko huo.

Mafunzo hayo ya siku mbili yaliyoanza Agosti 17, 2026, yalifunguliwa na Meneja wa PSSSF Kanda ya Kinondoni, Bw. Costa Mpagike, kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF, Bw. Fortunatus Magambo.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Bw. Mpagike alisema lengo kuu ni kujenga na kuimarisha uhusiano wa kudumu kati ya PSSSF na vyombo vya habari ili kuwezesha utoaji wa taarifa sahihi kwa umma kuhusu masuala ya hifadhi ya jamii.

“Kama mjuavyo, mafunzo haya ya siku mbili yanalenga kujenga na kuimarisha uhusiano wa kudumu na vyombo vya habari pamoja na waandishi wa habari, kuongeza uelewa wa umma na wanachama kuhusu shughuli za PSSSF, haki na wajibu wao kupitia mada mbalimbali za mafunzo, uzalishaji wa makala za uchambuzi na kupunguza upotoshaji wa taarifa” alisema Bw. Mpagike.

Aliongeza kuwa mbali na kuwapatia maarifa kuhusu mifumo na huduma za PSSSF, Mfuko unatamani washiriki wa mafunzo hayo wawe mabalozi wa kueneza taarifa sahihi za hifadhi ya jamii katika vyumba vya habari na kwenye jamii kwa ujumla.

“Tutawajengea uwezo ili muwe na taarifa sahihi kuhusu PSSSF na huduma zake, jambo ambalo litawarahisishia kuandika habari kwa ukweli, weledi na usahihi zaidi,” alisisitiza.

Baadhi ya washiriki walieleza kufurahishwa na fursa hiyo ya mafunzo, wakisema elimu waliyoipata itawasaidia kuboresha kazi zao za uandishi wa habari, hususan katika kuripoti masuala ya hifadhi ya jamii.

Mratibu wa mafunzo hayo, Bw. Nevile Meena, amesema elimu waliyoipata iwasaidie katika shughuli zao za uandishi wa habari.

“ Kama hujui kitu huwezi kuandika kwa usahihi, kama unafahamu jambo utaandika kwa usahihi, nawashukuru PSSSF kwa kutujengea uelewa, mimi binafsi nimekuwa mwandihi wa habari wa siku nyingi lakini kuna vitu vingine nimevifahamu sasa kujifunza hakuna mwisho. Naamini tutayatendea haki haya mafunzo na tutafanya vizuri katika kazi zetu.” Amesisitiza Bw. Meena

Mwandishi wa habari kutoka Kampuni ya Magazeti ya Serikali (TSN), Bi. Zena Chande, alisema mafunzo hayo yamemsaidia kuongeza uelewa kuhusu huduma na mafao yanayotolewa na PSSSF.

“Kimsingi nimeongeza uelewa kuhusu namna PSSSF inavyotekeleza majukumu yake. Mambo tuliyojifunza hapa yatanisaidia kufanya kazi yangu kwa ubora zaidi. Kabla ya mafunzo haya sikuwa na uelewa wa kutosha kuhusu kiinua mgongo, pensheni na sifa za kufaidika na mafao hayo, lakini sasa nimeelewa kwa kiwango kikubwa,” alisema Bi. Chande.

“ Ni mafunzo yenye tija kubwa sana kwetu sisi waandishi wa habari ambao tuna nafasi kubwa ya kuwasiliana na jamii wakiwemo wanachama wa PSSSF,” amesema Bi. Julieth Robert, mwandishi wa habari wa ITV.

Kwa upande wake, mwandishi wa habari mkongwe ambaye kwa sasa ni mnufaika wa pensheni kutoka PSSSF, Bw. Beda Msimbe, alitoa ushuhuda kuhusu umuhimu wa pensheni katika maisha ya mstaafu.

“Hii pensheni inanisaidia sana katika maisha yangu ya kila siku. Baada ya kustaafu, changamoto za maisha zipo, lakini mimi ninafurahia kuwa mwanachama wa PSSSF. Sasa ni mstaafu ninayepokea pensheni kila mwezi. Kila inapofika tarehe 22 napokea ujumbe mfupi wa simu unaonijulisha kuwa fedha zimeingizwa kwenye akaunti yangu. Kwa kweli, PSSSF wanatekeleza jukumu lao vizuri,” alisema Bw. Msimbe.

Mafunzo hayo ni sehemu ya mkakati wa PSSSF wa kuendelea kushirikiana na wadau mbalimbali, hususan vyombo vya habari, katika kuelimisha umma kuhusu umuhimu wa hifadhi ya jamii na huduma zinazotolewa na Mfuko huo.





Na Janeth Raphael - MichuziTv


Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 ya kujenga Tanzania yenye uchumi wa kisasa, jamii yenye ustawi, huduma bora za kijamii pamoja na matumizi makubwa ya teknolojia na ubunifu, imeelezwa kuwa inahitaji Serikali za Mitaa imara, zenye uwezo na zinazowajibika ili kuhakikisha malengo hayo yanafikiwa kwa ufanisi na kwa usawa.

Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Dkt. Jafar Seif, amesema ugatuzi wa madaraka katika mamlaka za Serikali za Mitaa ni nyenzo muhimu ya kufanikisha Dira hiyo, kwa kuwa unawawezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika maamuzi na utekelezaji wa shughuli za maendeleo katika maeneo yao.

Dkt. Seif ameyasema hayo leo jijini Dodoma wakati akifungua Mkutano Mkuu wa 16 wa Taasisi ya Maboresho katika Mamlaka za Serikali za Mitaa (TOA), unaofanyika chini ya kaulimbiu isemayo “Ugatuzi wa Madaraka katika Mamlaka za Serikali za Mitaa ni Nyenzo Madhubuti ya Kufikia Dira ya Taifa 2050.”

Amesema ugatuzi wa madaraka si suala la kiutawala pekee, bali ni msingi wa kuwapa wananchi nafasi ya kushiriki katika maamuzi yanayohusu maendeleo yao, akieleza kuwa Serikali za Mitaa ndizo zilizo karibu zaidi na wananchi na zina nafasi kubwa katika kuhakikisha huduma na miradi ya maendeleo inawafikia kwa wakati.

“Serikali za Mitaa zikiwa imara na zenye uwezo wa kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, Taifa linaweza kufikia malengo yake kwa haraka zaidi na kwa usawa,” amesema Dkt. Seif.

Amesema Serikali imepanga kuchukua hatua zaidi katika eneo la ugatuzi wa madaraka kwa kuimarisha mifumo mbalimbali ya kiutendaji na usimamizi, hususan katika eneo la fedha, hatua inayolenga kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa miradi na utoaji wa huduma kwa wananchi.

Dkt. Seif amesema kwa sasa fedha za utekelezaji wa miradi ya maendeleo zinapelekwa moja kwa moja katika taasisi za Serikali zilizopo ngazi za chini, ikiwemo shule, zahanati, ofisi za kata, vijiji pamoja na maeneo mengine ya kiutawala na kiutendaji.

Ameeleza kuwa hatua hiyo inalenga kuhakikisha rasilimali zinazotengwa kwa ajili ya maendeleo zinawafikia walengwa moja kwa moja na kutumika katika kutatua changamoto zinazowakabili wananchi katika maeneo yao.

Aidha, Dkt. Seif amesema ili Dira ya Taifa ya 2050 ifikiwe, Serikali za Mitaa zinapaswa kuimarisha maeneo muhimu ikiwemo uongozi bora na uwajibikaji, mipango madhubuti ya maendeleo, usimamizi wa rasilimali za umma, ushirikishwaji wa wananchi pamoja na matumizi ya TEHAMA katika utoaji wa huduma.

Amesema TOA imeendelea kuwa jukwaa muhimu la kuwakutanisha viongozi na wataalamu wa Serikali za Mitaa kwa ajili ya kubadilishana uzoefu, kujifunza na kutafuta suluhisho la changamoto zinazojitokeza katika ngazi za chini za utendaji.

Dkt. Seif amesisitiza kuwa mafanikio ya ugatuzi wa madaraka yanategemea kwa kiasi kikubwa uwezo wa taasisi kujenga mazingira ya uwazi, uwajibikaji na ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu ya Serikali za Mitaa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TOA, Albert Msovela, amesema taasisi hiyo itaendelea kushirikiana na Serikali katika kusimamia maendeleo ya wananchi na kuimarisha utawala bora, huku akisisitiza umuhimu wa kuendelea kujenga uwezo wa mamlaka za Serikali za Mitaa ili ziweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.

Mkutano huo wa 16 wa TOA unajadili masuala mbalimbali yanayohusu maboresho ya utendaji wa Serikali za Mitaa, ugatuzi wa madaraka na namna ya kuimarisha utoaji wa huduma kwa wananchi katika kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050.







Top News