Na Janeth Raphael - MichuziTv

WAZIRI wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, ameitaka Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) kuimarisha mfumo wa udahili na usajili wa wanafunzi wa elimu ya juu ili kuhakikisha vyuo havipokei wanafunzi zaidi ya uwezo wa miundombinu na wakufunzi waliopo.

Prof. Mkenda amesema hatua hiyo ni muhimu katika kulinda ubora wa elimu ya juu nchini, huku ikihakikisha wanafunzi wanapata nafasi za masomo kwa haki, uwazi na kwa kuzingatia uwezo halisi wa kila chuo.

Waziri huyo ameyasema hayo leo, Septemba 5, 2026, jijini Dodoma, baada ya kukutana na Makamu Wakuu wa Vyuo Vikuu pamoja na Wenyeviti wa Mabaraza ya vyuo vikuu nchini katika kikao kilichojadili masuala mbalimbali yanayohusu sekta ya elimu ya juu, ikiwemo udahili na usajili wa wanafunzi.

Amesema Serikali inalenga kuhakikisha mfumo wa udahili unakuwa bora na wenye ufanisi, ili kuepusha changamoto zinazoweza kujitokeza pale vyuo vinapodahili wanafunzi wengi kuliko uwezo wa kuwahudumia.

“Tumefanya hivyo kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunatengeneza mfumo mzuri ambao hautaleta utata, hautakuwa na kuweka idadi ya wanafunzi kuliko uwezo wa kufundisha,” amesema Prof. Mkenda.

Prof. Mkenda amewataka wanafunzi wanaotarajia kujiunga na vyuo vikuu kuendelea kufanya maombi yao wakati wakisubiri maelekezo zaidi kutoka TCU kuhusu utaratibu wa udahili.

Amesema mfumo unaoandaliwa unalenga kuweka uwiano kati ya ongezeko la mahitaji ya elimu ya juu na uwezo wa vyuo kutoa elimu bora, huku maslahi ya wanafunzi yakilindwa.

Serikali kuongeza nafasi za elimu ya juu

Waziri Mkenda amesema Serikali inaendelea kuongeza uwezo wa vyuo vikuu nchini kupitia ujenzi na upanuzi wa kampasi katika mikoa mbalimbali ili kuongeza nafasi za wanafunzi kupata elimu ya juu.

Amesema uwekezaji huo utawezesha vijana wengi zaidi kupata fursa za masomo bila kulazimisha vyuo kupokea idadi kubwa ya wanafunzi ambayo inaweza kuathiri ubora wa elimu.

Kwa mujibu wa Prof. Mkenda, Tanzania bado haijafikia kiwango cha uandikishaji wa wanafunzi katika elimu ya juu kinacholengwa, hivyo Serikali itaendelea kuongeza nafasi za masomo sambamba na kuhakikisha viwango vya elimu vinadumishwa.

Amesema lengo ni kujenga mfumo wa elimu ya juu unaotoa fursa kwa vijana wengi zaidi na wakati huo huo kuwaandaa kwa ufanisi ili waweze kukidhi mahitaji ya soko la ajira




TCU YAWEKA MKAZO KWENYE UDAHILI WA 2026/2027

Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa TCU, Prof. Charles Kihampa, amesema kikao hicho kimejadili kwa kina masuala ya udahili wa wanafunzi, ubora wa elimu pamoja na hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali katika kuendeleza sekta ya elimu ya juu.

Amesema TCU, Serikali na vyuo vikuu wamekubaliana kuendelea kushirikiana katika kuboresha mifumo ya udahili kwa kuzingatia mabadiliko na mahitaji yanayoendelea katika sekta ya elimu.

Prof. Kihampa amesema ongezeko linalotarajiwa la wanafunzi kutokana na mabadiliko mbalimbali ya sera linahitaji maandalizi ya mapema kutoka kwa Serikali, TCU na vyuo vikuu ili kuhakikisha uwezo wa kutoa elimu unaendana na idadi ya wanafunzi wanaotarajiwa.

Naye Mwenyekiti wa Baraza la Chuo Kikuu cha Teolojia cha Lweru, Aggrey Mlimuka, amesisitiza umuhimu wa vyuo vikuu kusimamia ubora wa elimu na kuhakikisha wahitimu wanakuwa na maarifa, uwezo na weledi unaokidhi mahitaji ya soko la ajira.

Amesema kila chuo kina wajibu wa kuhakikisha programu zake zinazalisha wataalamu wenye uwezo, akibainisha kuwa endapo ubora hautasimamiwa, soko la ajira litawachuja wahitimu kwa kuzingatia uwezo wao.

DIRISHA LA PILI LA UDAHIL KUFUNGULIWA WIKI IJAYO

Awali, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Ushirika Moshi (MoCU), Prof. Alfred Sife, amesema vyuo vikuu vimekubaliana kuendelea kuboresha mchakato wa udahili kwa mwaka wa masomo 2026/2027 ili kuhakikisha wanafunzi wanaodahiliwa wanakidhi vigezo na wanajiunga na programu zinazolingana na sifa zao.

Prof. Sife amesema moja ya hoja kubwa iliyojadiliwa katika kikao hicho ni mwenendo wa udahili unaoendelea, ambapo dirisha la kwanza la maombi limekamilika na dirisha la pili linatarajiwa kufunguliwa wiki ijayo.

Amesema kuimarishwa kwa mfumo huo kutasaidia kuhakikisha wanafunzi wenye sifa wanapata nafasi katika programu na vyuo vinavyowafaa, huku taratibu, kanuni na sheria za udahili zikizingatiwa.

Ameongeza kuwa ushirikiano kati ya Serikali, TCU na vyuo vikuu ni muhimu katika kuboresha mifumo ya elimu na kuhakikisha uwekezaji unaofanywa katika sekta hiyo unazalisha wahitimu wenye uwezo wa kukidhi mahitaji ya taifa na soko la ajira.



▪️︎ Aelekeza fedha zinazookolewa kwenye kubana matumizi zielekezwe kwenye huduma za wananchi

▪️︎ Aagiza magari ya kubeba wagonjwa yawe na mafuta, aonya wanaowachangisha wagonjwa

▪️︎ Ampongeza Afisa Elimu aliyesimamia shule kuongoza kitaifa


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali imejipanga kufanya mageuzi makubwa katika sekta ya elimu, ikiwemo kuhakikisha kila kijiji kinakuwa na shule ya sekondari, na zaidi ya vyumba 16,000 vya madarasa vikitarajiwa kujengwa ili kukidhi ongezeko la wanafunzi.

Dkt. Mwigulu amesema hayo leo, Jumamosi, Septemba 05, 2026, wakati akizungumza na wananchi wa Wilaya ya Bahi, mkoani Dodoma, katika Viwanja vya Halmashauri ya Bahi, alipokuwa katika ziara ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo, kuwasikiliza wananchi na kushughulikia changamoto zinazowakabili.

Amesema uamuzi wa kuongeza muda wa elimu ya lazima hadi kidato cha nne unaleta mahitaji makubwa ya miundombinu ya elimu, yakiwemo madarasa, maabara na maktaba.

“Tunaposema elimu ya lazima itakuwa mpaka kidato cha nne, maana yake tunasema kila kijiji kiwe na sekondari. Tunaongelea mahitaji ya madarasa zaidi ya vyumba 16,000.”

Waziri Mkuu amesema Serikali haitaki kuona watoto wakirejea katika mazingira ya kusoma chini ya miti, kukosa madarasa au kusoma katika mazingira ya msongamano, akisisitiza kuwa maandalizi ya mapema ni muhimu kukabiliana na mahitaji hayo.

Amesema Serikali pia inahitaji kuongeza idadi ya maabara, akieleza kuwa mahitaji yanaweza kufikia takribani maabara 8,000, pamoja na maktaba, ili kuimarisha mazingira ya kujifunzia na kufundishia.

Aidha, Dkt. Mwigulu amewataka viongozi wa Serikali kubadili baadhi ya taratibu zinazoweza kuokoa fedha na kuelekeza rasilimali hizo kwenye huduma zinazogusa maisha ya wananchi moja kwa moja.

Amesema viongozi wanapaswa kuweka mbele wajibu wa kuleta maendeleo kuliko kutafuta sifa zinazohusisha gharama zisizo za lazima.

Ametoa mfano wa misafara mikubwa ya viongozi na mikutano inayohusisha idadi kubwa ya watendaji kusafiri kwenda vituo vingine, akisema fedha zinazoweza kuokolewa zinapaswa kuelekezwa katika ujenzi wa madarasa, maabara, madawati na huduma nyingine muhimu.

“Kila tunapoweza kupata akiba tuielekeze kwenye jambo linalogusa maisha ya wananchi wetu ya kila siku.”

Kuhusu huduma za afya, Waziri Mkuu amewataka viongozi kuhakikisha magari ya kubeba wagonjwa ya Serikali yanakuwa na mafuta na wagonjwa wanaohitaji rufaa hawalazimishwi kuchangisha fedha kwa ajili ya mafuta.

Amesema Serikali imewekeza kwa kiasi kikubwa katika ujenzi wa hospitali, vituo vya afya, ununuzi wa magari ya kubeba wagonjwa, vifaa tiba na ajira za wataalamu, hivyo watendaji wanapaswa kuhakikisha uwekezaji huo unawanufaisha wananchi.

Ameonya kuwa mtumishi anayemlazimisha mgonjwa au ndugu yake kuchangisha fedha kwa ajili ya mafuta ya gari la kubeba wagonjwa anapaswa kuchukuliwa hatua, huku akiwataka wananchi kuripoti watumishi wanaokiuka taratibu na kuwanyima wananchi huduma wanazostahili.

Dkt. Mwigulu pia amempongeza Mkuu wa Divisheni ya Elimu ya Awali na Msingi, Boniface Wilson Mwakasole, kwa utendaji wake katika kuboresha elimu wilayani Bahi, akieleza kuwa amefuatilia kazi yake na kubaini mafanikio yaliyopatikana, ikiwemo Shule ya Msingi Chiona kuongoza kitaifa katika elimu ya msingi.

Amesema watendaji wanaofanya vizuri wanapaswa kutambuliwa na kupewa majukumu makubwa zaidi yanayolingana na uwezo wao.

Akimtolea mfano Boniface Wilson Mwakasole, Waziri Mkuu ameelekeza kuwa endapo mtendaji huyo ataondolewa Bahi, apandishwe cheo na kupewa jukumu kubwa zaidi kutokana na utendaji wake.

“Huyo mtu mzuri wa aina hiyo kama mnataka kumhamisha, mpandisheni; mpeni mkoa kama mnataka kumtoa Bahi. Kama hamjapata mkoa, msimhamishe, mbakizeni hapa hapa. Amefanya kazi nzuri ya kuigwa.”

Amesema utendaji mzuri unapaswa kuwa msingi wa kumpa mtumishi majukumu makubwa, akisisitiza kuwa mtu anayefanya kazi vizuri hahitaji kuomba nafasi kwa kutumia ushawishi kwa sababu kazi yake yenyewe inamtambulisha.“Mtu anayefanya kazi nzuri wala hahitaji lobbying, hauhitaji kuomba-omba kazi; kazi inakutambulisha.”

Amesema Serikali inapaswa kuwa na utamaduni wa kutambua na kupongeza watendaji wanaofanya vizuri, sambamba na kuchukua hatua kwa wale wanaoshindwa kutimiza wajibu wao.

Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kutekeleza miradi ya maendeleo katika Wilaya ya Bahi, ikiwemo miradi ya maji, afya, elimu, umwagiliaji, barabara na madaraja.

Amesema amepokea mahitaji mbalimbali yaliyowasilishwa na viongozi wa wilaya na mkoa na amemtaka Naibu Waziri anayesimamia Serikali za Mitaa kuyafuatilia kwa karibu ili hatua zichukuliwe katika maeneo yenye uhitaji.

Pia ameeleza kuwa maeneo yanayounganisha miji na vijiji, lakini wananchi wake bado wanaishi katika mazingira ya vijijini, yataendelea kunufaika na utaratibu wa kuunganishiwa umeme kwa gharama zinazotumika maeneo ya vijijini.









Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Dkt. Mahmoud Thabit Kombo (Mb), amekutana na kuagana na Balozi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Mheshimiwa Jean Pierre Massala, ambaye amehitimisha muda wake wa uwakilishi hapa nchini.

Mhe. Kombo alikutana na Balozi huyo Septemba 4, 2026, katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.

Katika kikao hicho, Waziri Kombo alimpongeza Balozi Massala kwa mchango wake katika kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na ushirikiano wa pande mbili kati ya Tanzania na DRC, hususan katika maeneo ya maendeleo, biashara na uwekezaji.

Waziri Kombo alisema Tanzania imeazimia kuimarisha zaidi ushirikiano wa kimkakati na DRC katika sekta mbalimbali, zikiwemo uchukuzi, madini, mafuta na gesi, ulinzi na usalama, pamoja na kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya pamoja yenye manufaa kwa wananchi wa nchi hizo mbili.

Miongoni mwa miradi ya kipaumbele ni ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR), inayolenga kuunganisha Tanzania na DRC kupitia Burundi, pamoja na ujenzi wa Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano ya Mawimbi ya Mwanga kutoka Kigoma nchini Tanzania hadi Kalemie, Mkoa wa Tanganyika nchini DRC, kupitia Ziwa Tanganyika.

Aidha, Tanzania na DRC zimekubaliana kuharakisha uanzishwaji wa Tume ya Pamoja ya Kiuchumi (JEC), ambayo inalenga kurahisisha utekelezaji wa miradi ya pamoja na kutengeneza fursa mpya za kiuchumi kwa nchi hizo.

Kwa upande wake, Balozi Massala ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa ushirikiano alioupata katika kipindi chake cha uwakilishi nchini na kusisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano wa kimkakati katika sekta mbalimbali za maendeleo kati ya Tanzania na DRC.















-Awapa maelekezo kwa Wakuu wa Mikoa, Wilaya na wakurugenzi wa halmashauri


Na Said Mwishehe,Michuzi TV

WAZIRI wa Nchi,Ofisi ya Makamu wa Rais-Muungano na Mazingira Mhandisi Hamad Yusufu Masauni ametoa mwito kwa Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa Halmashauri na Wenyeviti wa Serikali za Mitaa kuweka utaratibu kusimamia utekelezaji wa maelekezo ya kila Jumamosi ya mwisho wa mwezi kuwa siku ya usafi wa Mazingira Kitaifa.

Ametoa mwito huo leo Septemba 5,2026 aliposhiriki ufanyaji usafi katika Soko la Buguruni Jijini Dar es Salaam, Septemba 5, 2026 ambapo amefafanua Serikali kupitia Rais Dk.Samia Suluhu Hassan akiwa Makamu wa Rais mwaka 2016 alitoa agizo kuwa kila Jumamosi ya mwisho ya mwezi kuwa siku ya usafi wa Mazingira Kitaifa.

Aidha amesema Ofisi ya Makamu wa Rais ilitoa ‘Enviromental Management (Designation of National Cleanliness Day) Guidelines , 2016,chini ya G.N.No.139. Mwongozo huo unaelekeza utekelezaji wa tamko la Serikali la kuitangaza kila jumamosi ya mwisho wa Mwezi kuwa siku ya usafi wa Mazingira Kitaifa.

Mhandisi Masauni amesema kwa muktadha huo, Serikali inatoa mwito kwa Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa Halmashauri, Wenyeviti wa Serikali za Mitaa, Vijiji na Vitongoji kuhakikisha kuwa wanaweka utaratibu wa kusimamia utekelezaji wa maelekezo haya kwa kuzingatia maslahi ya makundi mbalimbali.

Amesisitiza ni wajibu wa kila mwananchi, mfanyabiashara, mwekezaji, taasisi za Serikali, sekta binafsi, viongozi wa mitaa, wenye viwanda, watoa huduma za taka, taasisi za elimu na jamii kwa ujumla kuwa na utaratibu wa kufanya na kusimamia Usafi wa Mazingira katika maeneo yao.

“Hivyo Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inamtaka kila Mtanzania kushiriki katika usafi wa mazingira.” Amesema Mhe. Masauni.Taka zinapotupwa hovyo, mifereji inapoziba, maeneo ya biashara yanapokuwa machafu au taka ngumu na hatarishi zinaposhughulikiwa bila utaratibu, madhara yake huonekana katika afya ya wananchi, miundombinu, mito, bahari na uchumi.”

Waziri Masauni amesema Mazingira machafu yanaweza kuchangia kuenea kwa magonjwa, kuongeza gharama za usafi na afya, kupunguza mvuto wa miji yetu kwa watalii na wawekezaji, na kuharibu rasilimali ambazo Watanzania wanategemea kwa maisha yao.

Pia amesema usimamizi wa taka hususan katika maeneo ya mjini hairidhishi ambapo wastani wa asilimia 37 tu ya taka ngumu zinazozalishwa hukusanywa na hivyo kiasi kikubwa cha taka huzagaa.

Kwa upande mwingine amesema, taka zinaweza kuwa fursa ya kiuchumi kupitia urejelezaji uchumi rejeshi, taka kutumika kama chanzo cha uzalishaji wa Nishati, Uzalishaji wa mbolea (mboji) na biashara ya kaboni.

Mathalani, Tanzania ina fursa ya uwekezaji wenye thamani ya takribani shilingi bilioni 22 kutoka katika taka plastiki, karatasi chakavu, taka za kielektroniki na betri chakavu.

Pamoja na hayo amewakumbusha kuwa Serikali ilishazuia matumizi ya mifuko ya plastiki kutokana na athari za kimazingira na ilishakaa kikao na wazalishaji wa mifuko hiyo kutengeneza mifuko ambayo ni rafiki wa mazingira ili wafanyabiashara watumie mifuko hiyo.

“Nimeona bado mifuko ya plastiki inatumiwa na baadhi ya wafanyabiashara,nawakumbusha mifuko ya plastiki tulishaizuia hivyo wanaotengeneza mifuko tunawakumbusha kuwa na mifuko mbadala badala ya kutengeneza mifuko ya plastiki.







Na Said Mwishehe,Michuzi TV


MKUU wa Wilaya ya Ilala jijini Dar es Salaam Edward Mpogolo, amesema wilaya hiyo inaendelea kutekeleza maagizo ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kuhusu uondoaji wa taka na usafi wa mazingira huku akisisitiza suala la usafi ni wa kila siku.

Pia amesema viongozi, wananchi, wafanyabiashara na viongozi wa masoko wameendelea kushirikiana kuhakikisha maeneo mbalimbali yanakuwa safi, hususan katika masoko makubwa yaliyopo wilayani Ilala.

Mpogolo ameyasema hayo leo Septemba 5,2026 wakati aliposhiriki usafi katika Soko la Buguruni akiungana na Waziri wa Nchi,Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhandisi Hamad Masauni,Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam Elihuruma Mabelya, viongozi, wafanyabiashara na wananchi.

Amesema katika Wilaya ya Ilala kuna masoko makubwa yakiwemo Soko la Samaki Feri, Soko la Kisutu, Soko la Buguruni na Soko la Ilala, akisisitiza kuwa usafi katika maeneo hayo ni jukumu la kila mmoja.

“Kama unavyojua Ilala ndiyo tuna masoko makubwa, hivyo nitumie nafasi hii pia kuwaelekeza viongozi wa masoko na wafanyabiashara kuhakikisha wanafanya usafi na kuyaweka masoko yao katika hali ya usafi,” amesema Mpogolo.

Ameongeza hatua zilizochukuliwa na wafanyabiashara zimeanza kuonekana, ambapo baadhi yao wamejitokeza kufanya usafi katika maeneo yao ya biashara na wengine wameondoa bidhaa zilizokuwa zimepangwa barabarani na kuzipeleka ndani ya masoko.

“Leo hii ninyi ni mashahidi, mmeona wafanyabiashara walioko mbele ya Soko la Buguruni ambao waliopanga barabarani wameondoa bidhaa zao kwa sababu wanatambua pia na wao walikuwa wanafanya makosa kufanyia biashara zao maeneo ya barabara,” amesema.

Mpogolo pia amewashukuru wananchi na wafanyabiashara wote waliojitokeza kushiriki katika zoezi la usafi, akisema Jiji la Dar es Salaam limeweka utaratibu wa kuhakikisha usafi unafanyika kila siku.

Amesema hatua hiyo inalenga kulirejesha jiji katika hali nzuri ya usafi na kulifikisha katika kiwango kinachoridhisha, sambamba na kutekeleza maelekezo ya Rais.

“Tumeshakubaliana kwamba tutahakikisha tunafanya usafi kila siku katika Jiji la Dar es Salaam ili lifike katika standard ambayo inaridhisha kama Rais Dk.Samia Suluhu Hassan alivyotuelekeza.Kwa sasa usafi kwa Dar es Salaam ni kila siku,” amesema.

Aidha, amewataka wananchi wote wa Ilala kuhakikisha kila mmoja anatimiza wajibu wake katika kutunza usafi kwenye maeneo yao ya biashara na makazi.

Pamoja na hilo, amewataka wafanyabiashara wanaopanga bidhaa zao barabarani kuondoa bidhaa hizo, akieleza kuwa maeneo hayo yamewekewa miundombinu maalumu kwa ajili ya watembea kwa miguu.

Mpogolo amesema Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam ameelekeza magari ya matangazo kwenda katika maeneo mbalimbali kutoa elimu na tahadhari kwa wafanyabiashara wanaopanga bidhaa zao barabarani ili waondoe.

“Katika barabara zile nimewekwa pavement, wako wapita kwa miguu ambao wanatakiwa kupita kwenye maeneo yale, lakini magari yanatakiwa kuendelea kupita vizuri,hivyo hatutarajii wafanyabiashara kupanga bidhaa zao barabarani.”

Amesisitiza usafi na matumizi sahihi ya maeneo ya umma ni wajibu wa kila mwananchi ili kuhakikisha Jiji la Dar es Salaam linakuwa safi, salama na lenye mazingira bora kwa shughuli za kila siku.











Mbunge wa Mbinga Vijijini na Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Judith Salvio Kapinga, akiambatana na Mkuu wa Wilaya ya Mbinga, Mhe. Kisare Makori, pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga, Joseph Kashushura, wamekutana na Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, Septemba 4, 2026, jijini Dodoma, kujadili changamoto zinazotokana na shughuli za uchimbaji wa makaa ya mawe mkoani Ruvuma.

Katika kikao hicho, viongozi hao waliwasilisha kero za wananchi kuhusu ulipaji wa fidia kwa wanaoathiriwa na shughuli za uchimbaji, utekelezaji wa Wajibu wa Kampuni kwa Jamii (CSR), pamoja na baadhi ya kampuni kutotekeleza kwa wakati wajibu mbalimbali unaohusiana na maeneo wanayofanyia shughuli.

Mhe. Kapinga amesema changamoto hizo zimekuwa zikigusa maisha ya wananchi, ikiwemo upatikanaji wa maji, barabara na huduma za afya, hivyo kuomba Wizara ya Madini kuchukua hatua kuhakikisha kampuni zinazofanya shughuli za uchimbaji zinatimiza wajibu wao kwa jamii.

Akijibu hoja hizo, Mhe. Mavunde ameahidi kuwa Wizara yake itashughulikia changamoto hizo ndani ya mwezi mmoja, huku akiiagiza Tume ya Madini kufika mkoani Ruvuma na kukutana na wamiliki wa migodi pamoja na wananchi kwa ajili ya kutafuta suluhu na kuhakikisha changamoto zinazohusiana na shughuli za uchimbaji zinapatiwa ufumbuzi.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Mbinga na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga wameshauri kuwekwa kwa mikakati madhubuti ya kukusanya madeni ya mapato yanayokaribia asilimia 70.







CHAANI, ZANZIBAR


NAIBU Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Ndg. Abdi Mahmoud Abdi, amesema CCM inaandaa mkakati imara wa kuimarisha uhai wa chama hicho ili kiendelee kudumu na kutoa mchango mkubwa kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.

Ndg. Abdi amesema hayo leo, Septemba 5, 2026, wakati akizungumza na viongozi pamoja na wajumbe wa Kamati za Siasa za Mkoa na Wilaya katika Jimbo la Chaani, Zanzibar.

Amepongeza hatua zinazochukuliwa na viongozi wa Jimbo la Chaani katika kuimarisha maendeleo ya chama na wananchi, akisisitiza umuhimu wa kuhakikisha rasilimali za chama zinasimamiwa kwa ufanisi na kutumika kwa manufaa ya chama, wananchi na Taifa.

Amesema moja ya malengo ya ziara yake ni kukagua mali za CCM na kujionea namna zinavyosimamiwa na kuendelezwa ili ziweze kutoa tija kwa chama na wananchi.

Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Chaani, Ndg. Ayoub Mohammed Mahmoud, amesema jimbo hilo lina mali mbalimbali zinazoweza kuchangia maendeleo ya CCM, ikiwemo fremu za maduka pamoja na miradi mingine ya maendeleo inayotekelezwa katika maeneo mbalimbali ya jimbo hilo.

Amesema viongozi wanaendelea na mpango wa ujenzi wa jengo la CCM litakaloendana na hadhi ya chama, huku likiwa na huduma mbalimbali pamoja na ukumbi mkubwa utakaotumika kwa shughuli za chama na shughuli za kijamii.

Hata hivyo, Mbunge huyo ametaja ukosefu wa miundombinu ya barabara za kisasa kuwa miongoni mwa changamoto zinazolikabili Jimbo la Chaani, akisema hali hiyo inarudisha nyuma kasi ya maendeleo katika baadhi ya maeneo.

Akitoa ufafanuzi kuhusu changamoto hizo, Ndg. Abdi amesema amezipokea na atazifanyia kazi kwa lengo la kuhakikisha zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati.

Awali, mara baada ya kuwasili Jimboni Chaani, Ndg. Abdi alipokea taarifa ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za jimbo hilo, ikiwemo miradi ya maendeleo ya chama na jitihada za kuwawezesha wananchi kiuchumi.

Taarifa hiyo pia imeeleza hatua zinazochukuliwa katika kuwawezesha vijana kupata elimu, kuboresha huduma za michezo pamoja na kuhamasisha ushiriki wa wananchi katika shughuli mbalimbali za maendeleo.


















Top News