Na Janeth Raphael -MichuziTv
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametoa wito kwa viongozi wa nchi za Afrika kuharakisha utekelezaji wa miradi ya miundombinu, akisisitiza kuwa maendeleo ya Bara hilo hayatapimwa kwa mipango na sera pekee, bali kwa matokeo yanayoonekana katika maisha ya wananchi.
Rais Samia ameyasema hayo leo jijini Dar es Salaam wakati akifungua Jukwaa la Miundombinu Afrika pamoja na Mkutano Mkuu wa Wanahisa wa Africa50, ambapo alieleza kuwa uwekezaji katika miundombinu ni nguzo muhimu ya kukuza uchumi, kuongeza ushindani wa Afrika, kuvutia wawekezaji na kuimarisha biashara ndani ya bara.
Amesema wananchi wanahitaji kuona matokeo kupitia ujenzi wa barabara bora, reli za kisasa, bandari zenye ufanisi, nishati ya uhakika, maendeleo ya teknolojia pamoja na kuongezeka kwa fursa za ajira.
Akizungumzia hatua zinazochukuliwa na Tanzania, Rais Samia alisema Serikali inaendelea kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kujenga uchumi wa viwanda, jumuishi na unaotegemea ubunifu, ujuzi pamoja na miundombinu ya kisasa.
Amebainisha kuwa Serikali imeendelea kuwekeza katika kuboresha Bandari ya Dar es Salaam, Reli ya Kisasa (SGR), barabara, madaraja na korido za kimkakati ili kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha biashara na usafirishaji katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika.
Rais Samia amesema uwekezaji huo hauwanufaishi Watanzania pekee, bali pia unahudumia nchi jirani zisizo na bandari, zikiwemo Burundi, Rwanda, Uganda, Zambia, Malawi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), hivyo kuimarisha nafasi ya Tanzania kama lango muhimu la biashara na uwekezaji barani Afrika.
Aidha, amesisitiza kuwa Afrika inapaswa kuongeza thamani ya rasilimali zake badala ya kuendelea kusafirisha malighafi, hatua ambayo itaongeza ajira, ujuzi na uwezo wa uzalishaji ndani ya bara.
Katika sekta ya nishati, Rais Samia alieleza kuwa gesi asilia ina nafasi kubwa katika kuimarisha usalama wa nishati, kusaidia ukuaji wa viwanda na kuchochea maendeleo ya uchumi wa Tanzania pamoja na nchi nyingine za Afrika.
Kwa upande wake, Naibu Rais wa Kenya, Prof. Kithure Kindiki, alisema mafanikio ya miradi mikubwa ya miundombinu yanategemea uongozi madhubuti wa kisiasa, sera thabiti na mipango ya muda mrefu.
Prof. Kindiki pia amezitaka nchi za Afrika kuwekeza katika kujenga uwezo wa wataalamu wa ndani, kutumia mifumo bunifu ya kugharamia miradi na kuhakikisha wananchi wanashirikishwa kikamilifu ili wanufaike na maendeleo yanayotekelezwa.
Naye Mwenyekiti wa Africa50 ambaye pia ni Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Dkt. Sidi Ould Tah, alisema taasisi hiyo itaendelea kusaidia nchi za Afrika kubadilisha fursa za miundombinu kuwa miradi inayoweza kufadhiliwa na kutekelezwa kwa ufanisi.
Amesema katika muongo wa pili wa Africa50, kipaumbele kitakuwa kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi, kuhamasisha mitaji na kuimarisha ushirikiano kati ya serikali, taasisi za fedha na sekta binafsi.
Mkutano huo pia ulihusisha mjadala wa mawaziri kutoka Tanzania, Msumbiji, Nigeria na Senegal kuhusu matumizi ya gesi asilia, maendeleo ya viwanda, kuongeza thamani ya rasilimali na ujenzi wa miundombinu ya kikanda.
Katika mjadala huo ilielezwa kuwa zaidi ya Waafrika milioni 600 bado hawana huduma ya umeme, huku Tanzania ikitajwa kuongeza upatikanaji wa nishati safi ya kupikia kutoka asilimia sita mwaka 2021 hadi asilimia 28 mwaka 2026.
Sambamba na mkutano huo, Tanzania ilisaini makubaliano mbalimbali ya ushirikiano yanayolenga kupanua huduma za matibabu ya figo, kuendeleza miradi ya usafirishaji wa umeme kwa ubia wa sekta ya umma na binafsi, pamoja na kuongeza matumizi ya gesi asilia katika shughuli za viwanda.
Makubaliano hayo yanahusisha Africa50, Wizara ya Afya, Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) pamoja na kampuni ya TAQA Arabia.
Akihitimisha hotuba yake, Rais Samia aliipongeza Africa50 kwa mchango wake katika kuendeleza ajenda ya miundombinu barani Afrika na kusisitiza kuwa makubaliano yote yaliyofikiwa yanapaswa kutekelezwa kwa haraka ili yaweze kuleta manufaa ya moja kwa moja kwa wananchi.




















.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)




.jpeg)





.jpeg)





.jpeg)




