Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Ndugu Abdi Mahamoud Abdi, ameendelea na ziara katika Jimbo la Tumbatu kwa lengo la kukagua uhai wa Chama, kusikiliza changamoto za wanachama na wananchi, pamoja na kuimarisha umoja na mshikamano ndani ya Chama.

Katika ziara hiyo, Ndugu Abdi ametembelea Matawi ya CCM ya Mkokotoni, Mto wa Pwani, Kiongele na Pale, ambako amezungumza na wanachama na wananchi kuhusu changamoto mbalimbali zinazowakabili katika maeneo yao.

Ndugu Abdi amewataka viongozi na wanachama wa CCM kuendelea kudumisha umoja na mshikamano, huku akisisitiza umuhimu wa wanachama kutimiza wajibu wao wa kulipa ada za Chama ili kuwezesha shughuli za CCM kutekelezwa kwa ufanisi kuanzia ngazi ya tawi hadi jimbo.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Wazazi CCM Zanzibar, Ndugu Ali Issa Ali, amesema ziara hiyo ni sehemu ya juhudi za kuimarisha umoja na mshikamano baina ya viongozi na wanachama kuanzia ngazi ya tawi hadi jimbo.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Ndugu Khadija Salum Ali, amesema Wizara inaendelea kuchukua hatua na kuweka mipango ya kuhakikisha changamoto zinazokabili sekta ya elimu katika maeneo ya Kiongele na maeneo mengine zinapatiwa ufumbuzi.

Aidha, Ndugu Abdi ametumia ziara hiyo kuwatembelea na kuwajulia hali baadhi ya Wazee wa Chama, hatua aliyoieleza kuwa ni sehemu ya kuendelea kujenga mshikamano, upendo na utamaduni wa kujali hali za wanachama na viongozi wa CCM.














Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Albert Chalamila amekutana na wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari nchini ikiwa ni mkakati wa Mkoa huo kuimarisha uelewa kwa wananchi kuhusiana na usafi jijini humo, tahadhari ya mvua za Elnino, upangaji wa wafanyabiashara wadogo pamoja na maandalizi ya kupokea wanafunzi wa kidato cha kwanza mwaka 2018 

Akizungumza leo Septemba 17, 2026 jijini Dar es Salaam na wahariri wa vyombo vya Habari RC Chalamila amesema moja ya mambo ambayo Mkoa huo umekusudia kuyafanya ili kuimarisha usafi ni pamoja na kubadili mitazamo ya wananchi ili wawe na utamaduni wa kupenda kufanya usafi na kutenganisha taka kwa kutumia wataalamu kuelimisha jamii pamoja na kusimamia sheria za usafi ipasavyo

Chalamila amesema kuwa katika mkakati huo pia wametoa muda wa miezi mitatu kwa wakandarasi wa uzoaji taka kuwa na vifaa vya kisasa na teknolojia inayoendana na uhitaji wa Mkoa huo, sanjari na kuwezesha usafi kufanyika nyakati za usiku na kuwa na mifumo bora ya uondoshaji maji taka ambapo pia amezungumzia mpango wa kutumia taasisi binafsi kufanya uchakataji taka kupata mbolea na bidhaa zingine.

Akizungumzia suala la wafanyabiashara wadogo RC Chalamila amesema Mkoa huo imeweka mikakati bora ya kuhakikisha biashara ikiwemo za mama lishe zinafanyika kwenye maeneo rasmi na kuondoka maeneo yasio rasmi huku akielekeza TANROAD kuimarisha upandaji miti na utunzaji bustani za barabarani na ametoa muda wa wiki mbili kwa barabara ya uwanja wa ndege (Nyerere Road)

Aidha Mkuu wa Mkoa amezungumzia tahadhari ya uwepo wa Mvua za Elnino kama zilivyotabiriwa na mamlaka ya Hali ya Hewa Nchini TMA na kusema kuwa ni muhimu kwa wananchi kuendelea kuchukua tahadhari kwa kutoziba mitaro, kuepuka utupaji taka hovyo, kusafisha mito sanjari na kuhifadhi chakula huku akisisitiza kuwa s Mkoa huo unaendelea kuboresha miundombinu

Vilevile Chalamila ameeleza mikakati ya Mkoa huo kwa kushirikiana na wadau wa Sekta binafsi kukabiliana na uwepo wa idadi kubwa ya wanafunzi wa kidato cha kwanza mwaka 2018 kutokana na mabadiliko ya mitaala ambapo mwaka 2017 darasa la sita na la saba watahitimu hivyo mbali na ujenzi wa madarasa unaoendelea pia madarasa ya shule binafsi yatatumika

Kwa upande wa Mwenyekiti wa jukwaa la wahariri Tanzania TEF Deudatus Balile amezungumzia taarifa za kidunia zinazoashiria uwepo wa majanga ya mvua kubwa huku akisisitiza usimamizi wa sheria kwenye kuimarisha usafi wa mazingira.













Na Mwandishi Wetu

‎RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, amepongezwa kwa kuwezesha Idara ya Uhamiaji kuendelea kuboresha na kuimarisha matumizi ya teknolojia za kisasa katika utoaji wa huduma za Uhamiaji, hatua inayolenga kurahisisha na kuongeza ufanisi katika taratibu za kuingia na kutoka nchini kwa raia na wageni.

Pongezi hizo zimetolewa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Patrobas Katambi na Kamishna Jenerali wa Uhamiaji CGI Dkt. Anna Makakala wakati wa uzinduzi wa darasa la mafunzo ya mfumo huo katika Chuo Cha Uhamiaji Cha Kikanda TRITA Moshi Mkoani Kilimanjaro Septemba 2026.

‎‎Katika hatua hiyo ya mageuzi ya kidigitali, Idara ya Uhamiaji inatarajia kuanza kutumia mifumo mipya ya kiteknolojia katika vituo vya kuingia na kutoka nchini, ikiwemo Mfumo wa Advanced Passenger Information System (APIS) na Passenger Name Record (PNR).

‎Pia mifumo hiyo itawezesha upatikanaji na uchakataji wa taarifa za abiria kwa njia ya kidigitali kabla na wakati wa safari, jambo litakalosaidia maofisa uhamiaji kupata taarifa muhimu kwa wakati na hivyo kuwezesha huduma za uingiaji na utokaji nchini kutolewa kwa uharaka na ufanisi zaidi.

‎‎Aidha hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuendelea kuwekeza katika teknolojia na mifumo ya kisasa inayolenga kuboresha huduma kwa wananchi na wageni, huku ikiimarisha taratibu za usimamizi wa mipaka na usalama wa Taifa.

‎Kupitia maboresho hayo, Idara ya Uhamiaji Tanzania inaendelea kujikita katika matumizi ya teknolojia ya kidigitali ili kutoa huduma bora, salama, zenye ufanisi na zinazokwenda sambamba na viwango vya kimataifa.

‎Mifumo hiyo mipya inatarajiwa kuanza kufanya kazi hivi karibuni katika vituo husika vya kuingia na kutoka nchini.



Na Abdallah Nassoro - MOI
TAASISI ya Tiba ya Mifupa na Ubongo Muhimbili (MOI) imeanza kutumia technolojia ya kisasa kutoa matibabu ya kibingwa ya upasuaji wa ubongo kwa wagonjwa wa kiharusi inayongeza ufanisi wa matibabu Kwa wagonjwa.

Mkurugenzi wa Upasuaji wa Ubongo MOI Dkt. Lemeri Mchome amesema leo Septemba 17, 2026 kuwa technolojia hiyo ni ya kwanza kutumika nchini na kwamba inakwenda kuleta mapinduzi katika matibabu ya kiharusi.

"Tunatoboa tundu ndogo kichwani na tunapitisha kifaa maalum chenye kamera, Ile kamera inakwenda kutuonyesha eneo ambalo damu imevilia na kutuwezesha kuitoa bila kuathiri sehemu nyingine" amesema Dkt. Lemeri

"Hii ndiyo teknolojia ya kisasa zaidi duniani na sisi kama taasisi hatuko nyuma, wagonjwa wa kiharusi hawana sababu ya kukimbilia nje ya nchi Kwa matibabu, huduma hiyo inapatikana MOI...kwasasa tunapokea wagonjwa watatu hadi watano Kwa siku, teknolojia hii inakuwa msaada wa matibabu bora" ameongeza

Naye Daktari bingwa wa Upasuaji wa Ubongo MOI, Dkt. John Mtei ambaye ameshiriki katika upasuaji wa kwanza kwa kutumia kifaa hicho amesema technolojia hiyo inaacha alama katika mapinduzi ya tiba ya Kiharusi nchini.

"Ufanisi wa matibabu ndiyo nyenzo muhimu katika matumizi ya technolojia hii, mgonjwa anafanyiwa upasuaji na kuondolewa tatizo lake kwa uhakika" amesema Dkt. Mtei

Taasisi ya MOI imeendelea kujikita katika kuleta afua mbalimbali hapa nchini za kuipunguzia Serikali mzigo wa kupeleka wagonjwa nje ya nchi kwa rufaa za gharama kubwa na pia kuendelea kuwa kituo cha weledi cha matibabu ya Mifupa na mfumo wa fahamu barani Afrika





MWENYEKITI wa Chama cha Wamiliki wa Mabasi Tanzania (TABOA), Abdallah Kiongozi, amesema kuingia kwa mabasi ya King Long katika soko la Tanzania ni fursa ya kuimarisha sekta ya usafirishaji kupitia teknolojia, ubora na ushindani.

Kiongozi amesema mabasi yanayoletwa katika soko la Tanzania yanapaswa kuzingatia mazingira ya barabara nchini, safari za masafa marefu, uimara, matumizi bora ya mafuta pamoja na kutoa huduma salama na yenye starehe kwa abiria.

Amesema usalama wa abiria unapaswa kupewa kipaumbele, huku akieleza kuwa ubora wa uhandisi, viwango vya usalama, teknolojia na muundo wa kisasa ni mambo muhimu kwa mabasi yanayolenga kuhudumia soko la Tanzania.

“Gharama za mafuta ni miongoni mwa gharama kubwa kwa kampuni za mabasi. Hivyo, basi lenye matumizi mazuri ya mafuta na utendaji mzuri linaweza kusaidia kupunguza gharama za uendeshaji na kuongeza ufanisi wa biashara,” amesema Kiongozi.

Aidha, ameitaka King Long kuwekeza katika huduma baada ya mauzo, ikiwemo vituo vya matengenezo, upatikanaji wa vipuri na wataalamu wa kiufundi nchini, huku akisisitiza umuhimu wa kampuni kusikiliza maoni na mahitaji ya wamiliki wa mabasi ili kuboresha huduma zake.

Kiongozi pia ameshauri kuanzishwa kwa mifumo rafiki ya upatikanaji wa fedha kwa wamiliki wa mabasi kwa kushirikiana na taasisi za fedha nchini, akisema si rahisi kwa waendeshaji wengi kulipa gharama yote ya basi kwa wakati mmoja. Amesema iwapo King Long itaunganisha ubora wa mabasi, dhamana, vipuri, huduma baada ya mauzo na uwezeshaji wa kifedha, itakuwa na nafasi ya kujenga uhusiano mzuri na waendeshaji wa usafirishaji nchini.

Kampuni ya usafirishaji ya Rasco imeeleza kuwa imekuwa ikitumia mabasi ya King Long tangu mwaka 2018, ikibainisha kuwa katika kipindi hicho imejionea ubora, uimara, starehe na ufanisi wa mabasi hayo katika huduma za usafirishaji.

Mwakilishi wa kampuni hiyo amesema kwa waendeshaji wa usafirishaji wa abiria, uchaguzi wa basi ni uamuzi muhimu unaozingatia ubora, usalama, uimara na uwezo wa gari kufanya kazi kwa ufanisi katika safari mbalimbali.

Amesema tangu waanze kutumia mabasi hayo, wameendelea kushuhudia maboresho yanayofanywa na King Long kupitia ubunifu na teknolojia ili kuendana na mahitaji ya sekta ya usafirishaji.

Ameongeza kuwa Rasco inajivunia kuhusishwa na chapa hiyo na kutambua mchango wake katika kukuza huduma za usafirishaji, hususan kwa kutoa mabasi yenye starehe na yanayokidhi mahitaji ya safari za masafa marefu.

Kwa mujibu wa mwakilishi huyo, uzoefu wa Rasco wa kutumia King Long kwa miaka kadhaa unaonyesha uimara na utendaji wa mabasi hayo, jambo linalowapa waendeshaji msingi wa kuzingatia ubora na ufanisi wanapofanya maamuzi ya ununuzi wa mabasi.

Amesema mabasi yanayotoa huduma bora, salama na yenye starehe yana umuhimu mkubwa katika kuhakikisha abiria wanafanya safari zao kwa usalama na faraja.

Kwa upande wake, Meneja Mauzo wa Kampuni ya King Long, Ally Bakari Mkali, amesema kampuni hiyo imejipanga kutoa huduma bora baada ya mauzo kwa wamiliki wa mabasi nchini Tanzania, ikiwamo msaada wa kitaalamu, matengenezo na upatikanaji wa vipuri halisi.

Akizungumza katika uzinduzi wa chapa hiyo nchini, Mkali amesema uhusiano na mteja hauishii katika ununuzi wa basi, bali unaendelea kupitia huduma za matengenezo na msaada wa kitaalamu. Amesema King Long inalenga kushirikiana na wataalamu wa ndani pamoja na wamiliki na waendeshaji wa mabasi ili kuhakikisha huduma na bidhaa zake zinaendana na mahitaji ya soko.

Amesema kampuni hiyo inalenga kuwa mshirika wa muda mrefu katika sekta ya usafirishaji Tanzania na Afrika Mashariki, kwa kutoa magari yenye uimara, usalama na faraja kwa wasafiri. Ameongeza kuwa mrejesho kutoka kwa wadau utasaidia kuboresha bidhaa na huduma, huku uzinduzi huo ukiwa mwanzo wa ushirikiano mpana zaidi katika soko la Tanzania.



















Top News