Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Katavi, imezindua Kamati ya Ushauri wa Kisheria ngazi ya Mkoa na Wilaya katika Mkoa wa Katavi. Uzinduzi huo umefanyika tarehe 8 Septemba, 2026 na kufuatiwa na kliniki ya Sheria bila malipo iliyoanza tarehe 7 Septemba, 2026 katika Viwanja vya Azimio Mpanda .

Uzinduzi wa Kamati za Ushauri wa Kisheria na Kliniki ya Kisheria bila malipo, ni dhamira ya dhati ya Serikali kupitia Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya kutatua migogoro, kutoa ushauri wa Kisheria kwa wananchi na elimu ya Kisheria bila malipo.

Akizungumza katika hotuba yake ya Uzinduzi, Mkuu wa Wilaya ya Mpanda Mhe. Jamila Yusuph, ameeleza kuwa jukumu la kutatua migogoro katika maisha ya watanzania sio la Serikali pekee ni jukumu la wadau wote wa maendeleo.

Mhe. Mkuu wa Wilaya amekuwa mgeni rasmi akimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe. Mwanamvua Hoza Mrindoko katika Uzinduzi wa Kamati za Kudumu za Ushauri wa Kisheria ngazi ya Mkoa na Wilaya zimezinduliwa mkoani Katavi, tarehe 8 Septemba , 2026, katika Viwanja vya Azimio, Mpanda.

Akizungumza katika hafla hiyo, amesisitiza umuhimu wa wananchi kutumia fursa zinazotolewa na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kupitia Kamati hizo pamoja na Kliniki ya Sheria ili kupata elimu, ushauri na ufafanuzi wa masuala mbalimbali ya kisheria.

Akitoa shukrani zake Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Hamza S. Johari, amesema kuwa kitendo cha kusogeza huduma ya ushauri wa kisheria kwa wananchi wa mkoa wa Katavi zinaenda kutatua changamoto walizonazo wananchi za kisheria.

“Namshukuru Mhe. Hamza Johari, Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na Ofisi yake na Kamati ya kudumu ya Ushauri wa Kisheria ya Mkoa wa Katavi kwa kushirikiana na Ofisi yangu, kuweza kufanikisha sherehe hii ya Uzinduzi wa Kamati ya Ushauri wa Kisheria na Kliniki ya Sheria bila Malipo Mkoa wa Katavi.” Amesema Mhe. Jamila Yusuph.







UJENZI wa bomba la gesi asilia lenye urefu wa kilomita 22 kutoka Kisemvule hadi Mbagala umeingia hatua muhimu, huku kampuni ya Rashal Energies Limited ikiongeza kasi ya kazi katika maeneo ya njia yanayoweza kuathiriwa zaidi na mvua kubwa.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mtendaji wa Rashal Energies Limited, Farhiya Warsame, mradi huo unaendelea kwa wakati na ratiba ambapo unatarajiwa kukamilika Januari 2027, huku timu za ujenzi zikielekeza nguvu katika eneo la kuvuka Mto Mzinga na Vikundu Marsh, kabla ya kuanza kwa mvua zinazotarajiwa za El Niño.

Ujenzi wa bomba hilo ulianza rasmi Julai 28, 2026, baada ya vibali na idhini zote za kisheria kukamilishwa Mei mwaka huu na timu za ujenzi kuanza maandalizi na kuhamasishwa Juni.

Warsame amesema hadi sasa takribani kilomita mbili za bomba zimeunganishwa, huku kilomita 1.5 zikiwa zimechimbwa mitaro. Sehemu zilizokamilika zimekwishawekwa kwenye mitaro, kufunikwa na kufanyiwa majaribio ya shinikizo.

Mradi huo unafadhiliwa kikamilifu kwa mtaji wa Watanzania na unatekelezwa na wataalamu na wakandarasi wa Kitanzania, kwa mujibu wa kampuni hiyo.

Baada ya kukamilika, bomba hilo litaunganisha zaidi ya viwanda 10 vilivyopo katika ukanda wa Kisemvule–Mbagala na gesi asilia inayosafirishwa kwa mabomba, kutoa huduma kwa kituo cha Dar es Salaam Rapid Transit (DART) Mbagala na kuwa msingi wa kituo kikuu cha CNG kitakachosaidia upanuzi wa mtandao wa gesi hiyo katika jiji la Dar es Salaam.

Aidha Warsame, amesema mradi huo umeandaliwa kuonyesha uwezo wa kampuni za Kitanzania kutekeleza miradi mikubwa ya miundombinu ya nishati kwa viwango vya kimataifa.

“Bomba hili linafadhiliwa na Watanzania, linaandaliwa kitaalamu na Watanzania na linajengwa na Watanzania kwa manufaa ya viwanda na kaya za Watanzania,” amesema Warsame.

Amesema mradi huo pia unalenga kujenga kizazi kipya cha wataalamu wa Kitanzania ambao wataweza kushiriki katika miradi mingine ya miundombinu ya gesi nchini.

Kwa mujibu wa Warsame, zaidi ya kujenga miundombinu, kampuni inawekeza katika kuwajengea uwezo mafundi wa kuchomelea mabomba, wapima ardhi na wahandisi wa Kitanzania, ambao ujuzi wao utaendelea kutumika katika miradi ya usambazaji wa gesi nchini kwa miaka ijayo.

Bomba hilo linatarajiwa kuwa na nafasi muhimu katika upanuzi wa miundombinu ya gesi asilia iliyobanwa (CNG) jijini Dar es Salaam.

Katika awamu ya kwanza, Kituo Kikuu cha CNG Mbagala (Mother Station) kitabanisha gesi moja kwa moja kutoka kwenye bomba kwa ajili ya kujaza magari.

Aidha, Kituo cha Vijibweni (Daughter Station) kitahudumiwa kwa kutumia malori maalumu ya kubeba gesi iliyobanwa, kwa lengo la kuhudumia eneo linalokua kwa shughuli za viwanda kuzunguka Kigamboni.

Awamu ya pili ya mradi inatarajiwa kuhusisha ujenzi wa vituo vingine vitano vya CNG katika maeneo mbalimbali ya Dar es Salaam, hatua inayolenga kuweka msingi wa mtandao mpana wa CNG katika jiji hilo.

Maendeleo hayo yanaweza kuongeza matumizi ya gesi asilia katika sekta ya usafiri, wakati Tanzania ikiendelea kutafuta njia za kuongeza matumizi ya nishati safi na yenye gharama nafuu zaidi.


Bomba hilo linajengwa katika maeneo yenye shughuli nyingi za kibinadamu, ambako tayari kuna miundombinu ya maji, umeme na mawasiliano, jambo linalohitaji umakini mkubwa wa kiufundi.

Mhandisi wa Bomba wa Rashal Energies Limited, Peter Shauribosho, amesema hadi sasa mradi huo haujasababisha uharibifu wa miundombinu ya wahusika wengine katika njia inayopita bomba hilo na hakuna kiunganishi cha bomba kilichokamilika ambacho kimelazimika kufanyiwa kazi upya.

“Kufanya kazi katika korido yenye shughuli nyingi kama Kisemvule–Mbagala hakutupi nafasi ya kufanya makosa. Kila kiunganishi tunachofanya lazima kiwe sahihi mara ya kwanza,” amesema Shauribosho.

Amesema timu za ujenzi kwa sasa zinaweka mkazo katika maeneo ya Mto Mzinga na Vikundu, kutokana na uwezekano wa maeneo hayo kuathiriwa zaidi na mvua.

Shauribosho amesema timu maalumu zimepelekwa katika maeneo hayo kuhakikisha kazi muhimu inakamilishwa kabla ya kuanza kwa mvua, huku kampuni ikiwa na matumaini ya kukabidhi bomba lililokamilika na kufanyiwa majaribio ya shinikizo ifikapo Januari 2027.

Mradi huo pia unaendana na juhudi za Serikali za kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.

Warsame amesema bomba hilo limebuniwa kwa kuzingatia uwezekano wa kuunganisha kaya katika siku zijazo na kusaidia utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia, uliozinduliwa na Rais Samia Suluhu Hassan Mei 2024, ambao unalenga kuhakikisha angalau asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.

Gesi asilia itakayotumika katika bomba hilo itatolewa na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC).

Kwa Tanzania, umuhimu wa mradi huo hauishii katika kusafirisha gesi kutoka Kisemvule kwenda Mbagala. Miunganisho ya viwanda, miundombinu ya CNG na uwezekano wa kuunganisha kaya vinaifanya bomba hiyo kuwa sehemu ya juhudi pana za kuongeza matumizi ya gesi asilia katika uchumi wa ndani.

Iwapo itakamilika kama ilivyopangwa, mradi huo utaunganisha kwa karibu zaidi rasilimali ya gesi asilia ya Tanzania na usafiri wa mijini, viwanda na kaya, huku ukitoa mfano wa nafasi inayoongezeka ya mtaji na utaalamu wa Watanzania katika utekelezaji wa miradi mikubwa ya miundombinu ya nishati.





Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita, Ndugu Karia Rajab Magaro, tarehe 08 Septemba 2026 amewataka viongozi wa Baraza la Mamlaka ya Mji Mdogo wa Katoro kuweka mikakati madhubuti ya kukabiliana na changamoto ya uchafu katika Mji wa Katoro.

Magaro ameyasema hayo katika kikao kilichofanyika Ukumbi wa Msenyenge Katoro. Kikao hicho kiliwahusisha Wenyeviti wa Vitongoji, Watendaji wa Kata, Madiwani wa Kata za Nyamigota na Katoro, Afisa Tarafa ya Butundwe pamoja na Timu ya Menejimenti ya Halmashauri. Kikao hicho ni sehemu ya mpango mkakati maalum wa usimamizi wa usafi wa mazingira Mji Mdogo wa Katoro.

“Tunawiwa ni lazima tujadili kwa upana na kutafuta ufumbuzi utakaotufanya tuendane na miji mingine. Mji wa Katoro unatambulika kitaifa hivyo ni vema katika nyanja zote tuonekane tunasonga mbele ili kuendana na hadhi yake,” amesema Magaro.

Aidha, Magaro ametoa wito kwa utekelezaji wa mpango huo kuanza mara moja kwa uwazi katika ukusanyaji wa taka pamoja na tozo. Amesema wananchi wanapaswa kuona matokeo ya moja kwa moja kati ya fedha wanazolipa na huduma za usafi wanazopata.

“Tusimamie sheria zilizopo na tuondoe hofu katika kutekeleza shughuli za usafi. Pia tuache mazoea kwa wazalishaji wakubwa wa taka,” ameongeza Magaro.

Kwa upande wake Afisa Taka Ngumu wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita, Bi. Winner Mwansite, amesema ukuaji wa kasi wa idadi ya watu pamoja na ongezeko la shughuli za kiuchumi umechangia kuongezeka kwa uzalishaji wa taka ngumu.

Mwansite amesema kwa sasa Mji wa Katoro unakadiriwa kuzalisha wastani wa tani 180 hadi 205 za taka ngumu kwa siku.

Naye Diwani wa Kata ya Nyamigota, Mheshimiwa Hadija Joseph Said, amesema wananchi wa Katoro ni waelewa na wako tayari kushirikiana ili kuufanya mji huo uwe msafi. Amesema wataendelea kukaa na mabalozi ili kuwawezesha kufanikisha zoezi hilo kwa kushirikiana na mzabuni katika kuwasimamia.

Kikao hicho kililenga kuweka mfumo endelevu, shirikishi na wenye kujiendesha kifedha wa usimamizi wa usafi wa mazingira katika Mji Mdogo wa Katoro. Mfumo huo utahakikisha taka ngumu zinakusanywa, kusafirishwa na kutupwa ipasavyo, huku gharama za uendeshaji zikitokana na ada na tozo za usafi zinazokusanywa.








Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhe. Stanslaus Haroon Nyongo, amesema ataendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wawekezaji ili kukuza uwekezaji na uchumi wa Mkoa wa Pwani, huku akisisitiza umuhimu wa kuwawezesha vijana kiuchumi.

Mhe. Nyongo amesema hayo leo, Septemba 8, 2026, wakati wa hafla fupi ya makabidhiano ya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani kati yake na aliyekuwa Mkuu wa Mkoa huo, Mhe. Abubakar Mussa Kunenge, ambaye kwa sasa ni Mkuu wa Mkoa wa Songwe.

Amesema Mkoa wa Pwani ni miongoni mwa maeneo muhimu kwa uwekezaji nchini na kwamba atashirikiana na viongozi na wadau mbalimbali kuhakikisha mazingira yanaendelea kuwa rafiki kwa wawekezaji.

“Mkoa huu ni wa uwekezaji. Nimezunguka maeneo mbalimbali kutafuta wawekezaji, kwa hiyo niwakaribishe kwa kuweka mazingira wezeshi,” amesema Mhe. Nyongo.

Aidha, Mhe. Nyongo ameomba ushirikiano wa jamii katika kuwajenga na kuwawezesha vijana kukabiliana na mabadiliko ya kiuchumi yanayolenga kuboresha maisha yao na jamii kwa ujumla.

Amesema atashirikiana na viongozi wa Mkoa katika kukuza uchumi kupitia sekta mbalimbali, ikiwemo kilimo, mifugo, uchumi wa buluu pamoja na sekta nyingine za uzalishaji.

“Ninaamini utendaji wetu wa pamoja utatumika kikamilifu katika kuendelea kuwatumikia wananchi kwa kutatua changamoto zao mbalimbali, pamoja na kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla,” amesema.

Katika hatua nyingine, Mhe. Nyongo ameomba viongozi na wananchi kutumia sheria, kanuni na taratibu katika kutatua migogoro ya ardhi, akisisitiza umuhimu wa kutumia busara na haki ili kupata suluhisho la kudumu.

Ameahidi kulisimamia kwa karibu suala hilo kwa lengo la kuhakikisha migogoro ya ardhi inapungua na wananchi wanapata haki na fursa ya kuendelea na shughuli zao za kiuchumi.

Rais wa Jamhuri ya Burundi, Mhe. Evariste Ndayishimiye, akimfariji Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, nyumbani kwake Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar, tarehe 08 Septemba 2026, kufuatia kifo cha mume wake, Marehemu Maalim Hafidh Ameir Hassan.


 

Mtume Boniface Mwamposa pamoja na Mchungaji Tony Kapola wakimfariji Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, baada ya kuwasili nyumbani kwake Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar, tarehe 08 Septemba 2026, kufuatia kifo cha mume wake, Marehemu Maalim Hafidh Ameir Hassan, aliyefariki dunia tarehe 07 Septemba 2026 katika Hospitali ya Kumbukumbu ya Emilio Mzena, Zanzibar.


 

Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Mhe. Felix Antoine Tshisekedi Tshilombo, akimfariji Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, alipowasili nyumbani kwa Rais Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar, tarehe 08 Septemba 2026, kufuatia kifo cha mume wake, Marehemu Maalim Hafidh Ameir Hassan, aliyefariki dunia tarehe 07 Septemba 2026 katika Hospitali ya Kumbukumbu ya Emilio Mzena, Zanzibar.


 

Na Mwandishi wetu, Dar

WAKULIMA wakubwa, wa kati na wadogo nchini wanatarajiwa kupata fursa zaidi ya kutumia teknolojia ya ndege nyuki katika shughuli za kilimo, ikiwemo kunyunyiza viuatilifu na kufuatilia afya ya mazao.

Hatua hiyo inakuja baada ya kampuni ya Mati Technologies Company Ltd na Mazao Hub kusaini hati ya makubaliano ya ushirikiano (MOU), kwa lengo la kuwawezesha wakulima, hususan wakulima wadogo, kupata huduma za teknolojia hiyo inayozalishwa nchini.

Akizungumza baada ya kusainiwa kwa MOU hiyo, Mkurugenzi wa Mati Technologies, Benjamin Mollel, amesema kampuni hiyo imekuwa ikishirikiana na majukwaa mbalimbali ya wakulima ili kupanua upatikanaji wa huduma za ndege nyuki na kuongeza tija katika kilimo.

Amesema Mazao Hub ni miongoni mwa majukwaa yanayowafikia wakulima wengi kupitia huduma zake za ugani na mfumo wa usambazaji wa pembejeo za kilimo, hivyo ushirikiano huo utasaidia kuunganisha wakulima na teknolojia kwa urahisi zaidi.

Mollel amesema lengo ni kuwafikia zaidi ya wakulima laki moja kote nchini ifikapo mwaka 2027, huku teknolojia hiyo ikilenga kusaidia wakulima kufanya kazi kwa ufanisi zaidi na kuongeza uzalishaji.

Kwa upande wake afisa mahusiano wa Mazao Hub Alexandra Ngaiza, amesema matumizi ya ndege nyuki katika kilimo yamekuwa yakihusishwa zaidi na wakulima wenye mashamba makubwa, lakini ushirikiano huo unalenga kubadilisha hali hiyo kwa kuwapa wakulima wadogo fursa ya kutumia teknolojia hiyo kupitia mifumo rahisi ya upatikanaji huduma ya Ndege nyuki hizo zinazozalishwa nchini.

Amesema teknolojia hiyo inaweza kusaidia kuongeza ufanisi katika unyunyiziaji wa viuatilifu, kuboresha uzalishaji na kupunguza uwezekano wa wakulima kukumbana moja kwa moja na kemikali wakati wa kunyunyizia mazao kwa njia za kawaida.

Mazao Hub, ambayo ni kampuni ya teknolojia ya kilimo (Agri-Tech), ambayo hutoa huduma za ugani kwa wakulima pamoja na kuwa na mfumo wa kuwaunganisha wakulima na pembejeo muhimu za kilimo, jambo linalowezesha teknolojia hiyo ya ndege nyuki zinazozalishwa nchini na Mati Technologies company ltd kuwafikia wakulima kupitia mtandao uliopo.


Red Cross Mkoa wa Simiyu imeendesha mafunzo maalum ya huduma ya kwanza kwa kushirikiana na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Simiyu. Mafunzo hayo yamefanyika tarehe 08 Septemba 2026 chini ya uongozi wa Mwenyekiti wa Red Cross Mkoa wa Simiyu, Sitta Tumma.

Lengo kubwa la mafunzo hayo ni kuwajengea uwezo watoa huduma wa kujitolea na askari wa zimamoto ili wawe tayari kutoa msaada wa haraka wakati wowote na mahala popote. Hii ni maandalizi ya kukabiliana na athari za mvua kubwa za El-Nino zinazotabiriwa kuanza Oktoba 2026.

Akizungumza baada ya mafunzo hayo, Red Cross Mkoa wa Simiyu ilisema imechukua jukumu la kuhakikisha jamii inakuwa tayari kukabiliana na majanga. Taasisi hiyo imesisitiza kuwa itaendelea kuimarisha utamaduni wa kujitolea kwa kuzingatia Kanuni Saba za Kimataifa za Red Cross ambazo ni Ubinadamu, Uadilifu, Kutokupendelea, Uhuru, Kujitolea, Umoja na Ulimwengu.

Katika mafunzo hayo ya pamoja, washiriki walipata elimu ya jinsi ya kutoa huduma ya kwanza kwa majeruhi, kuzuia damu, kutoa huduma kwa waliopata majeraha madogo na makubwa, pamoja na namna ya kuwasili katika tukio haraka na kwa usalama.

Watoa mafunzo walikuwa ni Hamis Shaban Mrisho, Barnabas Charles Daud, Aziz Abeod na Isaya Mganule. Walitoa masomo mbalimbali kwa vitendo na kinadharia ili kuhakikisha kila mshiriki anaelewa na anaweza kutekeleza.

Mafunzo haya yanakuja wakati Serikali ikitangaza kuwa mvua za El-Nino zinatarajiwa kuanza mwezi Oktoba na kuleta athari katika baadhi ya mikoa ikiwemo Simiyu. Hivyo ushirikiano kati ya Red Cross na Jeshi la Zimamoto unalenga kuhakikisha hakuna upotevu wa maisha utakaotokea wakati wa majanga hayo.














Serikali imesema udanganyifu katika mitihani ya kitaifa umepungua kwa kiasi kikubwa kutokana na kuimarishwa kwa usimamizi wa mitihani nchini.

Kauli hiyo imetolewa Septemba 7, 2026 mkoani Ruvuma na Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu Prof. Carolyne Nombo, alipofika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma na kuazungumzia utekelezaji wa masuala mbalimbali ya elimu ikiwemo maandalizi ya mtihani wa Taifa wa darasa la saba unaotrajia kufanyika nchini kote Septemba 9 na 10, 2026.

Ameeleza kuwa mitihani ya kitaifa ni suala nyeti linalohitaji usimamizi madhubuti, hivyo viongozi wa elimu katika ngazi zote wanapaswa kuhakikisha taratibu zote za mitihani zinafuatwa.

“Udanganyifu umepungua kwa kiasi kikubwa, nawasihi wanafunzi wa darasa la saba manaotarajia kufanya mitihani yenu kutojiingiza katika udanganyifu wowote wa mitihani, tuzingatie taratibu zote za mitihani,” amesisitiza Prof. Nombo

Aidha, amezitaka kamati za mitihani za mikoa na viongozi wa elimu kuendelea kushirikiana katika kusimamia mitihani, huku akiwapongeza kwa hatua ambazo tayari zimechukuliwa katika kupunguza udanganyifu.

Amebainisha kuwa, Serikali itaendelea kuchukua hatua pale inapobaini vitendo vya udanganyifu, hasa vile vinavyohusisha kupanga kwa pamoja kati ya wanafunzi, walimu au wasimamizi wa mitihani.

Kwa upande wake Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma ambaye ni Mkuu wa wilaya ya Songea Mhe. Wilman Kapenjama amesema mkoa umejiandaa vema katika kusimamia mtihani huo kwa hali ya usalama bila changamoto yoyote.

 

Vyama vya siasa nchini vimetakiwa kutumia majukwaa yao kuwahamasisha na kuwaelimisha wananchi kuhusu umuhimu wa kujiunga na Bima ya Afya kwa Wote, kwa kuwa afya ni haki ya kila mwananchi bila kujali itikadi, umri, jinsia au nafasi yake katika jamii.

Wito huo umetolewa na Kaimu Waziri wa Afya Dkt. Saada Mkuya Salum na Mbunge wa Welezo, wakati wa semina iliyowakutanisha wajumbe wa Baraza la Vyama vya Siasa na wataalamu kutoka Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) kwa ajili ya kuwajengea uelewa kuhusu Bima ya Afya kwa Wote.

Dkt. Mkuya alisema wanasiasa wana mtandao mpana wa kuwafikia wananchi kuanzia ngazi ya jamii hadi taifa, hivyo wana nafasi muhimu ya kuwa mabalozi wa elimu kuhusu afya na bima ya afya.

Alisema ushiriki wa vyama vya siasa katika kutoa elimu hiyo unaweza kusaidia kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa kuwa na bima ya afya na namna inavyoweza kusaidia kulinda afya na ustawi wa familia.

“Bima ya afya inalinda mwananchi na familia dhidi ya gharama kubwa za matibabu. Hili si suala la chama cha siasa, bali ni suala la maisha na ustawi wa wananchi,” alisema Dkt. Mkuya.

Aliongeza kuwa wanasiasa wanapokutana na wananchi katika maeneo mbalimbali, ikiwemo mikutano ya hadhara na majukwaa mengine, wanaweza kutumia fursa hizo kutoa elimu sahihi kuhusu umuhimu wa bima ya afya.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza la Vyama vya Siasa, Juma Ally Khatib, alisema elimu iliyotolewa katika semina hiyo itawafikia viongozi wa vyama vya siasa kuanzia ngazi ya taifa, mikoa, wilaya na kata, pamoja na wanachama wao.

Alisema viongozi hao watakuwa na jukumu la kuifikisha elimu hiyo kwa wananchi katika maeneo mbalimbali nchini, ili kuongeza uelewa na ushiriki katika mpango wa Bima ya Afya kwa Wote.

“Tunachojifunza hapa hakitaishia kwa wajumbe wa Baraza la Vyama vya Siasa. Tutakwenda kuwaelimisha viongozi wetu wa kitaifa, mikoa, wilaya, kata na wanachama, ambao nao wataifikisha elimu hii kwa wananchi,” alisema Khatib.

Naye Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa, Mohamed Ahmed, alisema semina hiyo inalenga kuwawezesha viongozi na wawakilishi wa vyama vya siasa kupata uelewa sahihi kuhusu mifumo ya bima ya afya nchini, ili waweze kutoa elimu sahihi kwa wananchi.

Alisema uelewa wa viongozi wa kisiasa ni muhimu kwa kuwa wana nafasi kubwa ya kuhamasisha wananchi kushiriki katika mipango mbalimbali ya Serikali inayolenga kuboresha upatikanaji wa huduma za afya.

Akizungumza katika semina hiyo, Dkt. David Mwanesano kutoka NHIF, alisema Serikali imeanza kutekeleza mpango wa Bima ya Afya kwa Wote kwa awamu, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha wananchi wanapata kinga dhidi ya changamoto za gharama za matibabu.

Alisema hadi sasa jumla ya kaya 276,400 zimekwishaandikishwa katika mpango huo na kuanza kupata huduma za afya.

Alisisitiza kuwa ushirikiano wa wadau mbalimbali, wakiwemo viongozi wa kisiasa, ni muhimu katika kufanikisha azma ya Serikali ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma za matibabu bila kukabiliwa na mzigo mkubwa wa gharama za matibabu.

Bima ya Afya kwa Wote, Jiunge Sasa


Top News