Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ameitaka Jumuiya ya Nchi za Afrika, Karibiani na Pasifiki (OACPS) kuhakikisha maazimio na matamko yanayopitishwa katika mikutano yake yanatekelezwa kupitia programu zenye manufaa ya moja kwa moja kwa nchi wanachama na wananchi.

Rais Dkt. Mwinyi ametoa wito huo leo, tarehe 23 Julai 2026, alipokutana na Katibu Mkuu wa OACPS, Mhe. Moussa Saleh Batraki na ujumbe wake , waliofika Ikulu Zanzibar.

Katika mazungumzo hayo, Rais Dkt. Mwinyi amesisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano katika maendeleo ya Uchumi wa Buluu, usimamizi endelevu wa rasilimali za bahari, uvuvi, uhifadhi wa mazingira ya bahari pamoja na kubadilishana uzoefu na teknolojia miongoni mwa nchi wanachama.

Ameeleza kuwa Zanzibar imeendelea kunufaika na programu mbalimbali zinazotekelezwa kupitia ushirikiano wa OACPS na Umoja wa Ulaya, zikiwemo programu zinazowawezesha wakulima wadogo kuboresha uzalishaji, kufikia viwango vya masoko na kuongeza ushindani wa mazao yao.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa OACPS, Mhe. Moussa Saleh Batraki, ameishukuru Tanzania kwa mchango wake katika shughuli za Jumuiya hiyo na kupongeza hatua zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuendeleza ajenda ya Uchumi wa Buluu. 

Halikadhalika, amesisitiza dhamira ya OACPS kuendelea kushirikiana na nchi wanachama katika kutafuta suluhisho la changamoto zinazokabili Mataifa Madogo ya Visiwa na kuimarisha maendeleo endelevu. 










Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Jeshi la Polisi Mkoa wa Dodoma linafanya uchunguzi wa tukio la mauaji ya Lea Eliud Mazengo (50), mkazi wa Kijiji cha Lamaiti wilayani Bahi, ambaye mwili wake ulipatikana ukiwa umefichwa shambani baada ya kutoweka kwa siku kadhaa.

Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa na familia, Lea aliondoka nyumbani Julai 20, 2026 kwenda shambani kwa ajili ya shughuli za kuvuna alizeti, lakini hakurejea nyumbani kama ilivyotarajiwa. Kutokana na kutopatikana kwake, ndugu pamoja na watoto wake walianza kumtafuta katika maeneo mbalimbali ya kijiji na mashambani.

Baada ya msako huo, mwili wa marehemu ulionekana ukiwa umefunikwa chini ya magunia ya alizeti yaliyokuwa shambani, hali iliyozua mshtuko mkubwa kwa familia na wakazi wa eneo hilo.

Akizungumza kuhusu tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, ACP Gallus Hyera, amesema uchunguzi wa awali unaonesha kuwa marehemu alifariki baada ya kukabwa shingoni. Amesema mtu anayehusishwa na tukio hilo ni aliyekuwa mume wake, huku chanzo kinachodaiwa kuchunguzwa kikitajwa kuwa ni wivu wa kimapenzi.

Mmoja wa wanafamilia ameeleza kuwa kabla ya tukio hilo, kulikuwa na migogoro ya kifamilia kati ya marehemu na mume wake, ikiwemo malalamiko yanayohusiana na mahitaji ya nyumbani na chakula. Aidha, amesema migogoro hiyo ilipelekea marehemu kuondolewa katika chumba walichokuwa wakilala na kuanza kutumia sebule kama sehemu yake ya kulala.

ACP Hyera amesema uchunguzi bado unaendelea ili kubaini mazingira yote yaliyopelekea kifo hicho na hatua zaidi za kisheria zitachukuliwa baada ya uchunguzi kukamilika.

Viongozi wa Kijiji cha Lamaiti wamemuelezea marehemu kuwa alikuwa kiongozi wa serikali ya kijiji na mwanajamii aliyekuwa akiheshimika kutokana na mchango wake katika shughuli za maendeleo ya kijiji. Tukio hilo limeacha simanzi kubwa kwa familia, viongozi na wakazi wa eneo hilo.



-Dkt. Numbi atoa somo kutoka Ghana kuhusu usimamizi wa ushirikishwaji wa wazawa katika Sekta ya Madini


📍MWANZA

Tume ya Madini imejipanga kuimarisha usimamizi wa ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini kwa kuhakikisha watoa huduma na wazalishaji wa bidhaa wanakidhi vigezo na viwango vya ubora vinavyohitajika, hatua inayolenga kuongeza mchango wa sekta hiyo katika ukuaji wa uchumi wa nchi.

Hayo yamesemwa leo, Julai 23, 2026, jijini Mwanza na Mwenyekiti wa Kamati ya Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini, Dkt. Theresia Numbi, kwenye Jukwaa la Tano la Utekelezaji wa Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini (LCCF 2026), linalowakutanisha wadau mbalimbali wa sekta hiyo.

Dkt. Numbi amesema Tume itaendelea kuboresha usimamizi wa eneo la ushirikishwaji wa Watanzania ili kuhakikisha wananchi wanapata fursa zaidi za kushiriki katika shughuli za uchimbaji wa madini, utoaji wa huduma, uzalishaji wa bidhaa na maeneo mengine ya mnyororo wa thamani wa Sekta ya Madini.

Akielezea uzoefu wa Ghana katika usimamizi wa ushirikishwaji wa wazawa, Dkt. Numbi amesema nchi hiyo imeweka mfumo madhubuti unaowataka waombaji wa fursa katika Sekta ya Madini kuwasilisha mipango ya ushirikishwaji wa wazawa, kulipa ada maalum na kurejesha sehemu ya fedha kwa Serikali kila mwisho wa mwaka.

Amesema mfumo huo pia unahakikisha watoa huduma wanakidhi vigezo vya kitaalamu na kuwa na uwezo unaohitajika kabla ya kupewa fursa ya kutoa huduma katika migodi ya madini.

Dkt. Numbi amewataka watoa huduma katika Sekta ya Madini kuhakikisha wanakidhi vigezo vinavyohitajika katika utoaji wa huduma na bidhaa migodini, sambamba na kuhakikisha bidhaa na huduma hizo zina ubora unaokidhi viwango vya juu.

“Ni muhimu kwa watoa huduma kuhakikisha wanakidhi vigezo vinavyohitajika na kutoa bidhaa na huduma zenye ubora unaokidhi viwango vya juu, kwa kuwa ubora ni msingi wa ushindani na uendelevu wa biashara katika Sekta ya Madini,” amesema Dkt. Numbi.

Aidha, amewataka Watanzania wanaoshiriki katika utoaji wa huduma na uzalishaji wa bidhaa kwa ajili ya migodi kuendelea kuimarisha uwezo wao, kuzingatia viwango vya ubora na kutumia teknolojia ili kuongeza ushindani na kunufaika zaidi na fursa zinazotokana na Sekta ya Madini.

Jukwaa hilo, ambalo leo limefikia siku yake ya pili, linaendelea kujadili masuala mbalimbali yanayolenga kuimarisha ushiriki wa Watanzania katika Sekta ya Madini, likiwemo suala la ushirikishwaji wa Watanzania katika Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGML), uzoefu bora kutoka kwa kampuni za Kitanzania zilizofanikiwa katika utekelezaji wa dhana ya ushirikishwaji wa Watanzania, pamoja na umuhimu wa kuzalisha rasilimaliwatu wenye ujuzi unaoendana na ukuaji wa teknolojia mpya katika Sekta ya Madini.

Vilevile, mdahalo maalum unajadili ajira, mafunzo na uhawilishaji wa teknolojia kama kichocheo cha kuongeza ushiriki na ujumuishaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini, sambamba na utekelezaji wa mipango ya urithishaji wa nafasi za kazi, changamoto zinazojitokeza na hatua zinazopaswa kuchukuliwa.

Jukwaa la LCCF 2026 limewakutanisha wadau mbalimbali wa Sekta ya Madini, wakiwemo makampuni ya uchimbaji wa madini, watoa huduma migodini, wafanyabiashara wa madini, wawekezaji, taasisi za umma na binafsi, pamoja na vyama vya wachimbaji wa madini nchini.

Jukwaa hilo linafanyika chini ya kaulimbiu: “Kutoka Majadiliano hadi Utekelezaji: Kujenga Sekta Imara ya Madini kupitia Ushirikishwaji wa Watanzania na Uanzishwaji wa Viwanda.”








Na Mwandishi Wetu

KATIKA kuunga mkono juhudi za Serikali za kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia, Oryx Gas Tanzania imetoa mafunzo ya matumizi salama na sahihi ya gesi ya kupikia kwa makundi ya wajasiriamali mbalimbali yakiwemo mama na baba lishe.

Mafunzo hayo yametolewa leo Julai 23,2026 katika Tamasha la Samaki Bagamoyo ambapo wajasiriamali zaidi ya 600 ambao wanashiriki tamasha hilo wamepatiwa mafunzo hayo kupitia maofisa wa Oryx Gas wakiongozwa na Meneja Mafunzo Peter Ndomba.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo Ndomba ametumia nafasi hiyo kuelezea amesema faida za kutumia LPG ikilinganishwa na nishati nyingine za kupikia, ikiwemo kupunguza gharama za uendeshaji, kuokoa muda wa kupika, kulinda afya kwa kupunguza moshi hatarishi, na kuhifadhi mazingira.

Pia amesema wajasiriamali na washiriki wa tamasha hilo wamejifunza mbinu bora za usalama zikiwemo ukaguzi wa mtungi, regulator na bomba kabla ya matumizi.

Nyingine ni namna ya kutambua uvujaji wa gesi na hatua sahihi za kuchukua,matumizi ya vifaa vilivyoidhinishwa na vyenye ubora,uhifadhi salama wa mitungi ya gesi, tahadhari za kuzuia ajali na hatua za kuchukua wakati wa dharura.

Aidha wamefundishwa mbinu bora za matumizi salama ya LPG katika shughuli za kila siku za upishi pamoja na athari za kuni na mkaa kwa mazingira na afya ya jamii hasa kwa kundi kubwa la wanawake ambao wanaathirika wa moshi wa kuni na mkaa kila siku.

“Kupitia mafunzo haya, Oryx Gas Tanzania inaendelea kuwawezesha wafanyabiashara wa chakula kutumia nishati safi kwa usalama, kuongeza ufanisi wa biashara zao na kuchangia afya bora pamoja na mazingira safi.

“Elimu ya matumizi salama ya LPG ni msingi wa kujenga jamii salama na kufanikisha ajenda ya taifa ya matumizi ya nishati safi ya kupikia.Oryx Gas Tanzania imekuwa kinara wa nishati safi na sasa imejikita pia kutoa elimu kwa makundi mchini Tanzaia ili kuhakikisha matumizi endelevu ya nishati safi.”










Serikali kupitia Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA) inaendelea kuimarisha uzalishaji na biashara ya zao la kitunguu kwa kukamilisha miongozo ya usimamizi wa zao hilo na kuendeleza miundombinu ya masoko, hatua zinazolenga kuongeza ushindani wa vitunguu vya Tanzania katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Akizungumza wakati wa ziara yake ya kikazi Wilaya ya Karatu, Waziri wa Kilimo, Mhe. Daniel Chongolo (Mb), ameielekeza COPRA kukamilisha miongozo ya zao la kitunguu ndani ya miezi mitatu na kuanza mchakato wa kupanua Soko la Vitunguu la Endashangwet ili kuongeza fursa za masoko kwa wakulima.

Akipokea maelekezo hayo, Mkurugenzi Mkuu wa COPRA, Bi. Irene Mlola, amesema miongozo hiyo ipo katika hatua za mwisho kukamilishwa na itaweka mfumo rasmi wa biashara ya vitunguu kupitia matumizi ya vipimo sahihi, vifungashio sanifu na usimamizi bora wa masoko.

Katika mwaka 2025/2026, Tanzania ilisafirisha kilogramu *33,295,659* za vitunguu zenye thamani ya zaidi ya *Shilingi bilioni 1.9*. Kupitia hatua hizi, Serikali inalenga kuongeza thamani ya zao, kupanua masoko ya kimataifa na kuongeza kipato cha wakulima. 





-Agusia tamaa ya maisha inavyochochea biashara dawa za kulevya kwa vijana

-Ataka vyombo vya ulinzi na usalama kuchunguza wenye Show room 


Na Said Mwishehe,Michuzi TV

MKUU wa Wilaya ya Temeke mkoani Dar es Salaam Sixtus Mapunda, amesema njia madhubuti ya kumaliza biashara ya dawa za kulevya nchini ni kukata cheni yote ya biashara hiyo kuanzia katika ngazi ya jamii ya kwenye mitaa huku akiitaka wananchi kushiriki mapambano dhidi ya dawa za kulevya.

Mapunda ametoa kauli hiyo leo Julai 23,2026 alipokuwa mgeni rasmi katika Tamasha laKufikia na kuhamasisha jamii dhidi ya madhara ya dawa za kulevya lililoandaliwa na Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya(DCEA).

Amesema pamoja na juhudi za kudhibiti uzalishaji, usafirishaji na uhifadhi wa dawa za kulevya, hatua hiyo bado ni ngumu kutokana na mbinu mbalimbali zinazotumiwa na wahalifu, hivyo jamii inapaswa kuelekeza nguvu zaidi katika kuzuia matumizi ya dawa hizo.

"Siku tusipokuwa na watumiaji, maana yake tumeshakata cheni. Kwenye biashara yoyote demand ndiyo inaleta supply. Ukikata uhitaji, mzigo utakosa soko," amesema.

Amesema wazazi wana wajibu wa kuanza kuwapa watoto elimu kuhusu madhara ya dawa za kulevya tangu wanapoanza kupata ufahamu ili kuwajengea uwezo wa kukataa vishawishi vinavyoweza kuharibu maisha yao.

Aidha, amewatahadharisha vijana kutojaribu kutumia dawa za kulevya kwa kudhani ni fasheni au starehe, akieleza kuwa uraibu huanza taratibu lakini madhara yake huwa makubwa na wakati mwingine hushindikana kurekebishwa.

“Nilipotembelea banda la Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya nimeoneshwa sampuli mbalimbali za dawa za kulevya ambazo zimetengenezwa kama keki ambazo zinazotumiwa na baadhi ya wanafunzi wa sekondari na vyuo vikuu katika sherehe binafsi.

“Tumefika katika hatua mbaya huko nyuma tulianza kama watumiaji baadae tukawa watumiaji na wasafirishaji lakini hivi sasa tumekuwa watengenezaji wa dawa za kulevya.Ni hatua mbaya sana na hivyo niwajibu wetu kukomesha dawa hizo kwa wote kushiriki katika mapambano.”

Amefafanua iwapo baadhi ya wanafunzi wa sekondari na vyuoni wameanza kutumia dawa za kulevya je hilo Taifa mbele ya safari bila kuchukua hatua hatma ya nchi itakuaje.

Katika hatua nyingine, amevitaka vyombo vya ulinzi na usalama kuendelea kufuatilia mitandao inayohusishwa na biashara haramu ya dawa za kulevya pamoja na mifumo ya utakatishaji fedha, akisema baadhi ya maisha ya anasa yasiyoelezeka yanaweza kuwa yanawavutia vijana kuingia katika biashara hiyo.

Ametoa mfano katika mitandao ya kijamii kuna baadhi ya watu wanaweka video wakionesha fedha bila kueleza walikozitoa jambo ambalo linalotia shaka na walikozipata na wanafanya hivyo kama sehemu ya kuhamasisha vijana kuingia kwenye maisha ya Misheni Town.

“Nilishasema katika Wilaya ya Temeke ni marufu wananchi kuonesha fedha katika mitandao ya kijamii na nikibaini tu huyo aliyeonesha hiyo video atamakatwa akahojiwe alikotoa hizo fedha maana fedha iliyotafutwa kwa jasho huwezi kuonesha.

“Nilimkamata cha kwanza nitawaambia TRA wakate kodi yao na kisha Polisi wamuweke mahabusu kwa ajili ya usalama wake maana anakaribisha wezi mtaani kwake.Lakini nyuma ya hizi video kuna mazingira ya kuhamasisha vijana kuingia kwa lengo la kutafuta maisha rahisi na matokeo yake unaingizwa katika biashara haramu kama ya dawa za kulevya.”

Pia amesema kwasasa mtaani kumekuwepo na maeneo mengi ya kuuza magari tena yenye gharama kubwa akitoa mfano uwepo wa Show room maeneo ya Buza au Mbagala.”Unajiuliza nani anaweza kununua BMW Buza?

“Sio kwamba nawatuhumu hapana lakini inatia mashaka na vyombo vya ulinzi mnaweza kwenda kuzungumza nao kirafiki tu.Isije ikawa mtu anatumia biashara ya magari kutakatisha fedha ambazo zimetokana na dawa za kulevya.”

Pia amewataka wananchi kutoa taarifa kuhusu watu wanaojihusisha na biashara ya dawa za kulevya badala ya kuwaficha, akisisitiza kuwa vita dhidi ya dawa za kulevya itafanikiwa pale jamii itakapokataa biashara hiyo kwa vitendo na si kwa maneno pekee.

Pamoja na hayo amesema mapambano dhidi ya dawa za kulevya yanahitaji ushirikiano wa serikali, wazazi, vijana na jamii kwa ujumla ili kulinda kizazi cha sasa na cha baadaye dhidi ya athari za janga hilo.









Na Benny Mwaipaja, London.

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amewakaribisha wawekezaji kutoka jumuiya ya kimataifa, kuchangamia fursa za uwekezaji nchini Tanzania katika sekta mbalimbali zikiwemo miundombinu, nishati, viwanda, kilimo, madini na huduma za kifedha.

Mhe. Balozi Omar ametoa wito huo jijini London nchini Uingereza alipoongoza ujumbe wa Tanzania katika Mkutano wa Kimkakati wa Uwekezaji na Ushirikiano wa Tanzania (Tanzania Strategic Investment and Partnership Forum) ukiwakutanisha viongozi wakuu wa taasisi kubwa za kifedha duniani, sekta ya bima na vihatarishi ulioandaliwa na Wizara ya Fedha kwa kushirikiana na Standard Bank ya nchini humo.

Alisema kuwa Serikali imeweka mazingira bora ya uwekezaji pamoja na vivutio vya kikodi ili kuvutia mitaji kutoka nje itakayochangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayoelekeza nchi ifikie uchumi wa dola za Marekani trilioni 1 ifikapo mwaka 2050 ambapo asilimia 70 ya fedha hizo zinatarajiwa kutoka sekta binafsi.

Awali, katika hotuba yake, Mhe. Balozi Omar aliwasilisha mwelekeo wa uchumi wa Tanzania chini ya Dira ya Maendeleo 2050, akibainisha kwamba uchumi wa Tanzania ulikua kwa asilimia 5.9 mwaka 2025, ukilinganisha na asilimia 5.5 mwaka 2024 huku Mfumko wa bei ukiendelea kubaki chini ya asilimia 5, miongoni mwa viwango vya chini zaidi barani Afrika;

Alisema kuwa nakisi ya bajeti imepungua hadi asilimia 3.1 ya Pato la Taifa; Karibu asilimia 74.2 ya bajeti ya Taifa sasa inagharamiwa na mapato ya ndani; Deni la Taifa linabaki himilivu kulingana na tathmini ya Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF.

Kwa upande wao, Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Standard Bank Ulaya na Mkurugenzi Mtendaji wa Standard Bank Tanzania, Bwana Ian Carson, alisisitiza dhamira ya benki hiyo ya kuendelea kuunganisha Afrika na masoko ya fedha ya kimataifa, akiitaja Tanzania kuwa miongoni mwa maeneo bora zaidi barani Afrika kwa uwekezaji wa muda mrefu.

Akizungumza wakati wa Mkutano huo, Balozi wa Tanzania nchini Uingereza, Mhe. Balozi Mbelwa Kairuki, alisema Serikali inaendelea kuwa na dhamira ya kudumisha mazungumzo ya mara kwa mara na jumuiya ya kimataifa ya wawekezaji.

"Tanzania inatekeleza mpango kabambe wa mageuzi ya kiuchumi unaojikita katika usimamizi imara wa uchumi mkubwa, mageuzi ya kimuundo na ushiriki wa sekta binafsi. Tunakaribisha ushirikiano endelevu na wawekezaji wa kimataifa kama washirika katika kufikia ukuaji wa uchumi endelevu na jumuishi," alisema Mhe. Balozi Kairuki.

Wawekezaji kadhaa walitaka ufafanuzi kuhusu mradi wa dola bilioni 42 wa Gesi Asilia Iliyogandamizwa (LNG) ambapo Mhe. Balozi Omar alieleza kuwa mazungumzo yamepiga hatua kubwa na masuala yaliyobaki ni ya ndani kati ya washirika wa kibiashara, huku Serikali ikiwa tayari kuendelea mara washirika hao watakapokamilisha michakato yao ya ndani.

Aidha, wawekezaji walionesha shauku kubwa kuhusu Reli ya Kisasa (SGR), Bandari za Dar es Salaam, Tanga na Mtwara, pamoja na njia za kibiashara za kikanda ambapo Serikali ilieleza kuwa ifikapo 2030/31, karibu kilomita zote 2,000 za mtandao wa SGR zitakuwa zimekamilika, hatua itakayoimarisha nafasi ya Tanzania kama lango kuu la kibiashara Afrika Mashariki.

Masuala mengine yaliyojadiliwa ni pamoja na upatikanaji wa fedha za kigeni, usalama wa nishati, uchumi wa kidijitali, kilimo na uongezaji thamani wa mazao kama pamba (mpango wa "Cotton-to-Cloth").

Mkutano huo, ambao ni sehemu ya jitihada endelevu za kidiplomasia za kiuchumi za Tanzania, uliongozwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Hamis Mussa Omar (Mb), akiambatana na Kamishna wa Usimamizi wa Deni la Serikali, Bwana Japhet Justine, huku Ubalozi wa Tanzania nchini Uingereza ukiwakilishwa na Mhe. Balozi Mbelwa Kairuki.


Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akizungumza wakati wa Mkutano wa Kimkakati wa Uwekezaji na Ushirikiano wa Tanzania (Tanzania Strategic Investment and Partnership Forum) uliowakutanisha viongozi wakuu wa taasisi kubwa za kifedha duniani, sekta ya bima na vihatarishi, ulioandaliwa na Wizara ya Fedha kwa kushirikiana na Standard Bank, Jijini London nchini Uingereza.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini-Wizara ya Fedha-London).








Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amezindua rasmi huduma za usafiri wa umma kwa kutumia mabasi ya umeme pamoja na Kituo cha Mabasi Malindi leo, tarehe 23 Julai 2026.

Katika hafla hiyo, Rais Dkt. Mwinyi ameitaka ZSSF kukamilisha kwa haraka ujenzi wa vituo vya kisasa vya mabasi ili wananchi wanufaike kikamilifu na huduma hiyo. Amesema mradi wa mabasi ya umeme utaboresha usafiri wa umma, kupunguza uchafuzi wa mazingira na kuongeza matumizi ya nishati safi.

Halikadhalika, Rais Dkt. Mwinyi  amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kutekeleza miradi mikubwa ya maendeleo ikiwemo barabara, maji, bandari, viwanja vya ndege, hospitali na Mji wa Michezo unaojiandaa kuhudumia mashindano ya AFCON, huku akiwataka wananchi kuilinda miundombinu ya umma na kuendelea kuunga mkono juhudi za maendeleo.

Hafla hiyo pia ilihusisha uzinduzi wa kadi maalumu za usafiri kwa wanafunzi, wazee na abiria wengine, hatua inayolenga kuboresha upatikanaji wa huduma za usafiri kwa makundi mbalimbali ya wananchi.













Top News