Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO) limezindua mfumo wa kidijitali wa TANFISH, unaolenga kuwaunganisha wavuvi, wasindikaji wa samaki na wanunuzi ili kurahisisha biashara ya mazao ya uvuvi na kuwafungulia wazalishaji masoko mapana zaidi ndani na nje ya maeneo yao

Akizungumza katika hafla hiyo iliyofanyika Dodoma, Mtaalamu wa Kimataifa  wa Mnyororo wa thamani wa Uvuvi na Ufugaji wa Viumbe  Maji wa FAO,  Hasheem Muumin, amesema TANFISH inawawezesha wavuvi na wasindikaji kujisajili kwenye mfumo, kuweka picha na taarifa za bidhaa zao na kuwasiliana moja kwa moja na wanunuzi kutoka maeneo mbalimbali nchini.

Amesema mfumo huo unahudumia aina mbalimbali za bidhaa za uvuvi, zikiwemo samaki wabichi, waliokaushwa na waliogandishwa kutoka kwenye maji ya bahari, maziwa pamoja na shughuli za ufugaji wa samaki.

Kwa mujibu wa  Muumin, TANFISH pia imejengwa kwa kuimarisha usalama wa miamala, ikiwemo kulinda malipo ya wanunuzi, huku ikiwawezesha wavuvi na wasindikaji kupata masoko makubwa na yenye uhakika zaidi.

“TANFISH inalinda malipo ya wanunuzi huku ikiwawezesha wavuvi na wasindikaji kupata masoko makubwa na yenye uhakika zaidi,” amesema Dkt. Muumin.

Amesema hadi sasa FAO imewapatia mafunzo zaidi ya wavuvi, wasindikaji na wadau wengine 500, ambao tayari wamesajiliwa katika mfumo huo.

Aidha, zaidi ya tani mbili za samaki tayari zimeuzwa kupitia TANFISH, huku Dodoma ikiwa miongoni mwa masoko makubwa yaliyofikiwa na mfumo huo pamoja na maeneo mengine nchini.

 Muumin amesema TANFISH ilianza kwa kulenga zaidi jamii zinazozunguka Ziwa Tanganyika, lakini sasa imepanuka na kuwajumuisha wasindikaji na wafanyabiashara kutoka Ziwa Victoria pamoja na maeneo ya pwani ya Tanzania, hatua inayolenga kujenga soko la kidijitali la bidhaa za uvuvi linalounganisha maeneo mbalimbali nchini.

Mfumo huo unapatikana kupitia vifaa vya Android na Apple, hivyo kuwawezesha watumiaji kuupata na kufanya biashara kwa urahisi zaidi.

Ili kuhakikisha ubora wa bidhaa na kulinda uaminifu wa watumiaji, wauzaji wanatakiwa kuzingatia matakwa yote ya kisheria na kanuni za Serikali, ikiwemo kuwa na nyaraka halali za biashara.

Kwa upande wa wanunuzi, wanatakiwa kutoa taarifa sahihi za mahali bidhaa zinapopaswa kufikishwa ili kurahisisha usafirishaji na kuhakikisha samaki wanafika kwa usalama na kwa wakati.

Uzinduzi wa TANFISH ni sehemu ya juhudi za FAO za kutumia teknolojia na mifumo ya kidijitali kuimarisha minyororo ya thamani ya kilimo na uvuvi, kuongeza fursa za masoko na kuchochea ongezeko la kipato kwa wazalishaji nchini.







Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) imeanza mazungumzo na wazalishaji wa parachichi katika wilaya za Mufindi na Njombe kwa lengo la kuanzisha mfumo wa ubunifu utakaoruhusu shamba kutumika kama ghala la bidhaa hai ili kuongeza ufanisi wa biashara ya zao hilo.

Mkurugenzi Mtendaji wa WRRB, Bw. Asangye Bangu, amesema hayo katika Maonesho ya Nanenane yanayoendelea kwenye Viwanja vya Dkt. John Malecela jijini Dodoma wakati akitoa maelezo kwa Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Denis Londo, aliyetembelea banda la WRRB.

Bw. Bangu amesema utaratibu huo utahakikisha matunda yanayovunwa ni yale tu yaliyofikia viwango vinavyohitajika na wanunuzi, jambo litakalopunguza upotevu wa mazao baada ya mavuno, kuhifadhi ubora wa bidhaa na kuongeza thamani ya biashara ya parachichi.

Aidha, amesema WRRB inatarajia kushirikiana na Shirika la Posta Tanzania ili kuunganisha Mfumo wa Stakabadhi za Ghala na huduma za kidijitali za biashara pamoja na usafirishaji wa bidhaa.

Amesema ushirikiano huo unatarajiwa kuongeza ufanisi wa biashara, kurahisisha miamala na kuimarisha imani ya wanunuzi katika soko.

Awali, Kaimu Mkurugenzi wa Uratibu Huduma wa WRRB, Bw. Mwita Thomas, amesema mfumo huo unaendelea kupanuliwa kutoka kwenye mazao ya kilimo pekee na sasa unahusisha pia bidhaa zisizo za kilimo, zikiwamo mifugo hai, mwani na samaki wanaofugwa kwenye vizimba.

Serikali mkoani Geita kupitia tume ya umwagiliaji  imesambaza jumla ya pampu 141 za umwagiliaji kwa vikundi 119 vya wakulima wenye takribani wanachama 13,000 katika halmashauri zote za mkoa huo, katika jitihada za kuongeza uzalishaji na kupunguza utegemezi wa mvua.

Akikabidhi pampu hizo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mkuu wa Wilaya ya Bukombe Paskas Muragili amesema pampu hizo zitaleta kasi kubwa ya uzalishaji kwa wakulima na kuchangia katika mapinduzi ya kilimo mkoani humo.

Ameongeza kuwa ugawaji wa pampu hizo unapaswa kwenda sambamba na ushirikishwaji wa sekta nyingine ikiwemo utoaji wa elimu na mbinu bora za kilimo na pia uhakikishaji wa upatikanaji wa pembejeo kwa wakati.

Kwa upande wake Mhandisi kutoka Timu ya Umwagiliaji mkoa wa Geita, Boniface Mkita amesema pampu hizo zimegharimu jumla ya shilingi bilioni 1.012.

Amefafanua kuwa kupitia mpango huu, eneo lenye ukubwa wa hekari 2,092 litamwagiliwa kwa wakati mmoja. Hii itapunguza utegemezi wa mvua na kupandisha uzalishaji wa zao la mahindi kutoka tni 1 kwa hekari hadi tani 2.5 kwa hekari1 

Mkita amebainisha kuwa mpango huu unatarajiwa kuwanufaisha moja kwa moja wakulima 1,389, kati yao wanawake 369 na wanaume 1,020.

 Serikali imesisitiza kuwa uwekezaji huu ni sehemu ya mkakati wa kuhakikisha Geita inakuwa miongoni mwa mikoa inayolisha Taifa kupitia kilimo cha umwagiliaji.








Na Belinda Joseph, Dodoma

Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dennis Londo, amesema matumizi ya taarifa sahihi za masoko ni nyenzo muhimu katika kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania, kukuza mauzo ya nje na kuvutia uwekezaji wa kimkakati unaochochea ukuaji wa uchumi.

Mhe. Londo ameyasema hayo Agosti 7, 2026, katika Viwanja vya Nane Nane, jijini Dodoma, wakati akifungua mkutano wa Intelijensia ya Masoko na Matokeo, ulioandaliwa na Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), uliowakutanisha wadau mbalimbali kujadili namna taarifa za masoko zinavyoweza kutumika kuchochea biashara na maendeleo ya viwanda.

Amesema mabadiliko ya teknolojia, mahitaji ya walaji na mifumo ya uzalishaji na usambazaji yanaendelea kufungua fursa mpya za biashara, hivyo Tanzania inapaswa kuendelea kutumia taarifa za masoko kuwawezesha wazalishaji na wafanyabiashara kufanya maamuzi sahihi na kuongeza ushindani katika masoko ya kikanda na kimataifa.

“Tunapaswa kuzalisha kwa kuzingatia mahitaji ya soko na kutumia taarifa sahihi za masoko katika kufanya maamuzi ya uzalishaji, uwekezaji na biashara,” amesema.

Ameeleza kuwa juhudi za Tanzania kujenga uchumi wa kisasa unaotegemea viwanda na kuongeza mauzo ya bidhaa nje ya nchi zinahitaji ushirikiano madhubuti kati ya Serikali, sekta binafsi na taasisi mbalimbali, ili kuhakikisha wazalishaji na wafanyabiashara wanapata taarifa muhimu za masoko kwa wakati.

Aidha, amesema Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa biashara na uwekezaji, pamoja na kuhamasisha uzalishaji wa bidhaa zenye ubora na viwango vinavyokidhi mahitaji ya masoko ya kimataifa, hatua itakayosaidia kuongeza thamani ya bidhaa na fursa za mauzo nje ya nchi.

Mhe. Londo amesema matumizi ya taarifa sahihi za masoko yatawawezesha wazalishaji kubaini mahitaji na fursa zilizopo katika masoko mbalimbali, kupanga uzalishaji kulingana na mahitaji ya walaji na kuimarisha uwezo wa bidhaa za Tanzania kushindana katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Amesisitiza kuwa mafanikio ya juhudi hizo yanahitaji ushirikiano wa karibu kati ya Serikali na sekta binafsi, huku akieleza kuwa kuunganisha taarifa za masoko na uzalishaji, uongezaji thamani na biashara kutasaidia kuongeza kipato cha wananchi, kutengeneza ajira na kuchochea ukuaji jumuishi wa uchumi.

Akihitimisha hotuba yake, Mhe. Londo amesema matumizi madhubuti ya taarifa za masoko, sambamba na uwekezaji katika uzalishaji na uongezaji thamani, ni msingi muhimu katika kujenga uchumi imara na wenye ushindani, huku Tanzania ikiendelea kutumia fursa zinazotokana na masoko ya kikanda na kimataifa.







Na Belinda Joseph-Dodoma.

Mkurugenzi wa Idara ya Uzalishaji na Maendeleo ya Masoko kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Stephen Michael, amesema Tanzania inalenga kuongeza uzalishaji wa maziwa na kuondokana na utegemezi wa uagizaji wa bidhaa za maziwa kutoka nje kupitia utekelezaji wa Mradi wa Mageuzi ya Tasnia ya Maziwa na Mabadiliko ya Tabianchi (C-SDTP).

Akizungumza na waandishi wa habari Agosti 7, 2026, katika Banda la C-SDTP kwenye Maonesho ya 88 yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Malecela jijini Dodoma, Stephen amesema sekta ya maziwa ni miongoni mwa sekta muhimu zinazochangia uchumi wa nchi kupitia sekta ya mifugo.

Amesema tathmini iliyofanyika imebaini kuwa ifikapo mwaka 2030 Tanzania inaweza kukabiliwa na upatikanaji mdogo wa maziwa endapo hakutakuwa na uwekezaji wa kutosha, kutokana na kuongezeka kwa kipato cha wananchi, ongezeko la idadi ya watu na kasi ya ukuaji wa mijini.

Kwa mujibu wa Stephen, Mradi wa C-SDTP wenye thamani ya dola za Marekani milioni 231 utatekelezwa kwa kipindi cha miaka 10, ukiwa na lengo la kuongeza uzalishaji wa maziwa, kuimarisha upatikanaji wa malighafi kwa viwanda vya kusindika maziwa na kuiwezesha Tanzania kubadilika kutoka kuwa muagizaji na kuwa muuzaji wa maziwa katika masoko ya nje.

Amesema mradi huo utatumia mfumo wa corridor approach katika maeneo yenye uwezo mkubwa wa uzalishaji wa maziwa, huku ukizingatia mnyororo wa thamani wa maziwa ili kuongeza uzalishaji, ukusanyaji, usindikaji na upatikanaji wa malighafi kwa viwanda.

Ameainisha kuwa mradi utatekelezwa katika mikoa ya Arusha, Iringa, Mbeya, Njombe, Tanga, Morogoro, Pwani na Kilimanjaro kwa Tanzania Bara, huku Zanzibar ukihusisha mikoa yote mitano ambayo ni Mjini Magharibi, Kaskazini Unguja, Kusini Unguja, Kaskazini Pemba na Kusini Pemba.

Stephen amesema mradi huo pia utatoa kipaumbele kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu kupitia upatikanaji wa ng’ombe bora wa maziwa kwa ruzuku, ujenzi wa vituo vya ukusanyaji wa maziwa (Milk Collection Centers na Milk Collection Points) pamoja na kuboresha miundombinu ya usafirishaji wa maziwa kutoka kwa wazalishaji kwenda viwandani.

Akizungumza Mratibu wa Mradi wa C-SDTP, Dkt. Lazaro Kapella, amesema ushiriki wa mradi katika Maonesho ya 88 ni fursa muhimu ya kukutana na wadau mbalimbali, kubadilishana uzoefu, kuonesha teknolojia na ubunifu wa ufugaji wa ng’ombe wa maziwa unaozingatia mabadiliko ya tabianchi, pamoja na kuimarisha ushirikiano katika maendeleo ya tasnia ya maziwa.

Amesema kupitia banda la C-SDTP, wananchi wanapata fursa ya kujifunza kuhusu teknolojia za uzalishaji wa malisho na lishe bora ya mifugo, huduma za afya na uboreshaji wa mifugo, ubora na usalama wa maziwa, uimarishaji wa masoko, huduma za kifedha na uwezeshaji wa vijana na wanawake.

Ameongeza kuwa mradi huo, unaotekelezwa kwa miaka 10 kuanzia 2024 hadi 2034 kwa ushirikiano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD), unalenga kujenga tasnia ya maziwa yenye tija, shindani, jumuishi na endelevu, ili Tanzania iweze kuongeza uzalishaji na hatimaye kuuza maziwa katika masoko ya nje.




📍Nzuguni : Dodoma

Waziri wa Kilimo, Mh.Daniel Chongolo, ameipongeza Tume ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC) na kuitaka kuhakikisha pampu za Umwagiliaji zilizotengwa kwa ajili ya wakulima zinagaiwa kuanzia Agosti 30 kwa wanufaika katika mikoa husika ili ziweze kutumika kuongeza uzalishaji wa mazao.

Chongolo ametoa maelekezo hayo leo alipotembelea banda la Tume ya Taifa ya Umwagiliaji katika Maonesho ya Wakulima (Nane Nane) yanayoendelea katika viwanja vya John Malechela, Nzuguni, mkoani Dodoma.

Amesema Serikali imeendelea kuwekeza katika upatikanaji wa teknolojia za Umwagiliaji kwa lengo la kuongeza tija ya uzalishaji, hivyo ni muhimu vifaa hivyo viwafikie wakulima kwa wakati ili viweze kutoa matokeo yaliyokusudiwa.

Waziri Chongolo amepongeza jitihada za Tume katika kuratibu na kusimamia utekelezaji wa programu mbalimbali za Umwagiliaji nchini, zikiwemo usambazaji wa pampu na utekelezaji wa miradi ya Umwagiliaji inayolenga kuwawezesha wakulima kuzalisha kwa ufanisi mwaka mzima.

Kwa upande wake, Salome Mallamia Mkurugenzi wa Uendeshaji wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji ameeleza kuwa Tume itaendelea kutekeleza maelekezo ya Serikali kwa kuhakikisha pampu hizo zinawafikia wakulima watakao nufaika ndani ya muda uliopangwa, hatua itakayochochea ongezeko la uzalishaji, kuinua kipato cha wakulima na kuendelea kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kupitia kaulimbiu ya “Tambua Soko, Ongeza Tija, Kutekeleza Dira 2050.













Aliiongoza Manonga kwa weledi mkubwa, ‘figisu’ ujumbe Kamati Utendaji Yanga wamtoa uongozini

Na Mwandishi Wetu

KATIKA Jamii yoyote, viongozi bora ni wale wanaotambua kwamba mafanikio ya kweli hupimwa kwa mchango wao katika kuboresha maisha ya wengine kwa namna moja au nyingine.

Miongoni mwa watu wanaotajwa kwa sifa nzuri za uongozi unaojengwa juu ya maadili, uwajibikaji na upendo kwa jamii ni pamoja na Seif Gulamali, kijana mpole ambaye amewahi kuliongoza Jimbo la Manonga kwa kipindi Cha awamu mbili tofauti, akitimiza majukumu yake ya kuwatumikia wananchi.

Kwa wasiomfahamu Gulamali, sifa yake kubwa ni uwezo wa kuwasikiliza watu na kuthamini mawazo yao bila ubaguzi wa aina yoyote na zaidi akiwa kiongozi aliyejijengea tabia ya kuwa msikilizaji wa masuala mbalimbali ya kijamii na hasa yale yanayogusa maisha ya watu.

Kupitia mwenendo wake, Seif Gulamali ameonyesha kuwa uongozi si mamlaka pekee, bali ni huduma kwa watu na kujitoa kwa ajili ya manufaa ya wengi pasipo kuwabagua kwa namna moja au nyingine kutokana na hali zao au nafasi zao za uongozi.

Aidha, anajulikana kwa kuamini katika mshikamano na ushirikiano akiendelea kuhamasisha watu kufanya kazi pamoja sambamba na kutatua changamoto kwa mazungumzo na kujenga umoja unaowezesha jamii kusonga mbele.

Upendo wake kwa jamii unaonekana katika namna anavyowathamini watu wa rika na makundi mbalimbali akitambua kuwa kila mtu ana nafasi ya kuchangia maendeleo, hivyo huwahimiza vijana kutumia vipaji vyao, huku akiheshimu mchango wa wazee na wanawake katika kujenga taifa lenye mshikamano.

Pia, Seif Gulamali ni mfano mzuri wa mtu anayesisitiza maadili, uadilifu na heshima kuwa ni moja ya uwajibikaji, hizi ni sehemu muhimu miongoni mwa sifa za uongozi unaodumu na unaoleta matokeo chanya kwa jamii akiamini kutenda haki hujenga imani kwa wananchi na kuimarisha ushirikiano katika kufikia malengo ya pamoja.

Akiwa Mbunge kwa wananchi wa Jimbo la Manonga,Seif Gulamali anaweza kutazamwa kama mfano wa uongozi unaozingatia utu, mshikamano na upendo kwa jamii, akishiriki katika masuala mbalimbali ya Kimaendeleo ulioliwezesha Manonga kupiga hatua.

Wakati wa Ubunge wake, Seif Gulamali ambaye ni Mwanachama Kindakindaki wa Klabu ya Yanga, pia amewahi kushika nafasi ya kuwa Mmoja wa Wajumbe wa Kamati ya Utendaji, akifanikiwa kuifanya timu hiyo ya Wananchi kupiga hatua kubwa na Muhimu ikiwemo kubeba nakuomba mbalimbali likiwemo la Ligi Kuu ambapo kwa msimu ulioisha imelibeba Taji hilo kwa mara ya 5 mfululizo.

Ameonyesha kuwa uongozi si nafasi ya kujinufaisha binafsi, bali ni dhamana ya kuhakikisha taasisi inapata maendeleo endelevu, sifa hizi ndizo zilizomfanya aonekane kuwa mmoja wa watu wanaoweza kutoa mchango mkubwa katika kuendelea kuijenga Yanga.

Pamoja na kutofanikiwa kupenya katika nafasi nne za Kamati ya Utendaji Yanga kwa madai ya uwepo wa Figisu licha ya jina lake kushika nafasi ya tatu, Gulamali ameendelea kuamini kuwa Yanga inaweza kufikia mafanikio makubwa zaidi ikiwa kutakuwa na ushirikiano, uwajibikaji na usimamizi makini wa rasilimali za klabu sambamba na umoja kutoka kwa kila Mwanachama.

Kimsingi mtazamo huu ni dhahiri kuwa unaonyesha dhamira yake ya kuona Yanga ikiendelea kuwa kinara ndani na nje ya Tanzania na kuziacha timu zingine zikiwa kama wasindikizaji katika malengo iliyojiwekea.

Aidha, Gulamali ni miongoni mwa viongozi ambao wamekuwa wakionesha mapenzi ya dhati kwa Yanga kwa muda mrefu huku ikiaminika kuwa Mapenzi yake ya kweli kwa klabu ni kuitumikia kwa moyo wote na kuhakikisha maslahi ya klabu yanatangulizwa mbele ya maslahi binafsi. 

Kwa miaka ya hivi karibuni, Gulamali amekuwa akitajwa miongoni mwa viongozi wanaoshiriki katika maendeleo ya Yanga na amewahi kueleza dhamira yake ya kusaidia kuisimamia klabu na kuendeleza mabadiliko ndani ya Yanga. Pia amewahi kuwa sehemu ya uongozi wa klabu hiyo kama mjumbe wa Kamati ya Utendaji, akichangia safari ya maendeleo ya Wanajangwani.

Wahenga Wana Usemi Usemao " Safari ni hatua" Yes na Kila jambo lina wakati wake, hatua ya kutopewa nafasi katika Kamati hiyo ya Utendaji Yanga, ukaribu wake na Kila mtu unatoa nafasi nyingi kwa Mwana Manonga kuendelea na hatua nyingine ingawa haina maana kuwa nafasi yake ya kuwatumikia wananchi ( Yanga) imefikia tamati.

Kwa wale tunaomtambua tunasema "Songa mbele" Mwamba Wananchi wa Manonga bado wanakuhitaji, "Songa mbele" Mwamba Wananchi wa Jangwani bado wanakutegemea"




Naibu Waziri, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray, amemtaka Mkandarasi wa mradi wa Mikocheni Apartments kuongeza kasi ya ujenzi ili kuhakikisha mradi huo unakamilika ifikapo Oktoba mwaka huu.

Mhe. Qwaray ametoa maelekezo hayo leo, Agosti 7, 2026 alipotembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa mradi huo jijini Dar es Salaam, ambao unasimamiwa na kumilikiwa na Watumishi Housing Investments.

Amesema Serikali inatarajia kuona Mkandarasi akiweka nguvu zaidi katika kukamilisha mradi huo kwa wakati ili watumishi wa umma ambao tayari wamelipia nyumba hizo waanze kuzitumia.

“Pamoja na kukamilisha mradi kwa wakati, Mkandarasi anapaswa kuzingatia viwango vya ubora wa ujenzi ili nyumba zinazojengwa zidumu na Serikali iweze na kuona thamani ya fedha iliyowekezwa” amesema.

Sambamba na hayo, Mhe. Qwaray ametoa wito kwa watumishi wa umma na wananchi wenye sifa ya kujiunga na Mfuko wa Faida Fund ili kujenga akiba ya muda mrefu itakayowawezesha kuwa na uhakika wa kifedha hapo baadaye.

Aidha, amesema kwa watumishi wa umma kujiunga na mfuko huo kutawasaidia kuongeza mafao yao ya uzeeni bila kuathiri mafao ya msingi yanayolipwa kupitia mifuko ya hifadhi ya jamii, huku akisisitiza kuwa uwekezaji wa mapema ni msingi wa ustawi wa kifedha.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Watumishi Housing Investments (WHI), Sephania Solomon, amesema maelekezo yote yaliyotolewa na Naibu Waziri wameyapokea na wataendelea kumsimamia mkandarasi ili ahakikishe anakamilisha mradi huo kwa wakati kama mkataba unavyoelekeza.

“Sisi maelekezo ya Waziri tumeyapokea na tutaendelea kumsimamia mkandarasi ili aweze kukamilisha nyumba hizi kwa wakati, kama mkataba unavyotaka,” alisema.












Yawataka wananchi kujiunga mapema kujikinga na gharama za matibabu

Na Grace Michael, Dodoma

MFUKO wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) umewahimiza wananchi nchini kujiunga na bima ya afya kabla ya kuugua, ukieleza kuwa ni njia salama ya kujikinga dhidi ya gharama kubwa za matibabu ambazo zinaweza kujitokeza wakati wowote.

Wito huo umetolewa leo Agosti 07, 2026 na Meneja Masoko na Huduma kwa Wateja wa NHIF, Angela Mziray, wakati akitoa elimu kwa wananchi waliotembelea banda la Mfuko katika Maonesho ya 49 ya Kilimo ya Nanenane yanayoendelea katika viwanja vya Nzuguni, mkoani Dodoma.

Bi. Mziray amesema maonesho hayo yameipa NHIF fursa ya kuwafikia wananchi wengi na kuwaelimisha kuhusu umuhimu wa kuwa na bima ya afya, sambamba na utekelezaji wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote inayolenga kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma za matibabu bila vikwazo vya kifedha.

Amesema changamoto za kiafya zinaweza kumpata mtu yeyote bila kutarajia, na mara nyingi husababisha familia nyingi kutumia akiba zao au hata kuuza mali ili kugharamia matibabu.

“Ugonjwa huja bila taarifa. Unaweza kuwa mzima leo lakini kesho ukahitaji matibabu ya gharama kubwa. Ndiyo maana tunawahimiza wananchi kujiunga na bima ya afya mapema ili wajenge kinga ya kifedha kwao na kwa familia zao," amesema Bi. Mziray.

Amefafanua kuwa mwananchi anapochangia bima ya afya kabla hajaugua, hupata uhakika wa matibabu bila kubeba mzigo mkubwa wa gharama wakati wa uhitaji.

“Ni muhimu wananchi wajidundulize kidogo kidogo na kuchangia bima ya afya. Hii ndiyo njia bora ya kuhakikisha familia inapata huduma za matibabu kwa wakati bila kuathiri mipango ya maendeleo," amesema.

Bi. Mziray amesema NHIF inaendelea kutoa elimu katika maeneo mbalimbali nchini ili kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu faida za bima ya afya na kuhamasisha matumizi ya mfumo wa bima badala ya kulipia matibabu moja kwa moja kutoka mfukoni.

Ameongeza kuwa wanachama wa NHIF wanapata huduma katika mtandao mpana wa vituo vya afya vya Serikali, binafsi na vya mashirika ya dini vilivyosajiliwa na Mfuko, jambo linalowapa urahisi wa kupata huduma popote wanapozihitaji.

Aidha, amesema kuwa na bima ya afya siyo tu kulinda afya ya mtu binafsi, bali pia ni kulinda uchumi wa familia kwa kupunguza matumizi yasiyotarajiwa yanayotokana na matibabu.

Katika Maonesho ya Nanenane, NHIF inaendelea kutoa huduma mbalimbali ikiwemo usajili wa wanachama wapya, elimu kuhusu vifurushi vya bima ya afya, ushauri kwa wanachama pamoja na ufafanuzi wa utekelezaji wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote.

Wananchi wanaotembelea banda la NHIF pia wanapata fursa ya kuuliza maswali, kupata majibu kuhusu huduma za Mfuko na kujiunga na bima ya afya papo hapo, hatua inayochangia kuongeza uelewa na ushiriki wa jamii katika kuhakikisha kila Mtanzania anakuwa na kinga ya kifedha dhidi ya gharama za matibabu.
Kaimu Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT) Mwl. Protas Magesa amefanya kikao maalum na watumishi wastaafu wa CWT, ikiwa ni kuthamini mchango wa waasisi na watumishi wastaafu wa chama waliowahi kutumikia kwa nyadhifa mbalimbali.

Kikao hicho kimefanyika leo katika Ukumbi wa Royal Village, jijini Dodoma, kikiongozwa na Kaimu Katibu Mkuu wa CWT, Mwl. Magesa Protas Magesa, akiambatana na Kaimu Mwekahazina wa CWT, Mwl. James Asagwile, pamoja na viongozi wa CWT Mkoa wa Dodoma.

Chama cha Walimu Tanzania, CWT, kimeendelea kuthibitisha dhamira yake ya kuthamini mchango wa watumishi wastaafu kwa lengo la kusikiliza ushauri, maoni na uzoefu wao kiutendaji kuhusu mustakabali wa chama na namna bora ya kuendelea kukijenga ili kiweze kuwahudumia wanachama kwa ufanisi zaidi.

Akizungumza katika kikao hicho, Mwl. Magesa amesema uongozi wa sasa unaamini kuwa uzoefu wa watumishi wastaafu ni hazina muhimu katika kuimarisha utendaji wa chama na miongoni mwa vipaumbele vya uongozi wake ni kuboresha huduma kwa wanachama na kutatua changamoto zilizodumu kwa muda mrefu, ikiwemo kuanza kulipa madeni ya mkono wa kwaheri pamoja na mabati kwa wastaafu.

Mwl. Magesa amesisitiza kuwa anatambua mchango mkubwa wa watumishi hao, wengi wao wakiwa sehemu ya waasisi walioijenga CWT tangu kuanzishwa kwake zaidi ya miaka 30 iliyopita na ameahidi kuendeleza maono yao kwa kuhakikisha chama kinaendelea kuwa imara, chenye mshikamano na kinachotetea maslahi ya walimu kwa ufanisi pia ni sehemu ya juhudi za uongozi wa CWT .

Kwa upande wake, Kaimu Mwekahazina wa CWT, Mwl. James Asagwile, amesema waasisi wa chama wameweka msingi imara uliowezesha kuzalisha viongozi wengi wanaoendelea kulitumikia taifa kupitia CWT. pia mebainisha kuwa uongozi wa sasa utaendelea kusikiliza ushauri wao na kwamba uzoefu wa watumishi wastaafu ni nguzo muhimu katika kuendelea kuijenga CWT.

Akizungumza kwa niaba ya watumishi wastaafu, Mwl. Dauda Bilikesi ameishukuru Ofisi ya Katibu Mkuu kwa kuandaa kikao hicho, akisema hatua hiyo imeonesha kuthamini mchango wa waliolitumikia chama kwa miaka mingi na kwasasa wastaafu wana matumaini makubwa ya kuona CWT ikiendelea kukua na kuimarisha nafasi yake katika kutetea na kuzungumzia maslahi ya walimu nchini.





Top News