Na Mwandishi Wetu
TEKNOLOJIA na matumizi jumuishi ya mtandao vinaweza kuwa nyenzo muhimu katika kuondoa vikwazo vinavyowakabili watu wenye mahitaji maalum katika elimu, ajira na kujiajiri, wadau wa Internet Governance wamesema.

Akizungumza katika mafunzo ya Tanzania School of Internet Governance, mtaalamu wa masuala ya Ujumuishwaji amesema Profesa Cosmas Mnyanyii watu wenye ulemavu, hususan wasioona na viziwi, bado wanakabiliwa na changamoto kubwa ya kupata ajira katika sekta mbalimbali, hali inayohitaji matumizi zaidi ya teknolojia kuwawezesha kujitegemea.

Amesema tafiti na uzoefu unaonyesha kuwa watu wenye ulemavu mara nyingi hujikuta wakifanya kazi chache zisizohitaji ujuzi mkubwa, hivyo teknolojia inapaswa kutumika kuwapa ujuzi unaowawezesha kushindana katika soko la ajira na kujiajiri.

Kwa mujibu wake, mafunzo ya matumizi ya kompyuta kwa wasioona na viziwi yameonyesha kuwa teknolojia inaweza kuwawezesha kufanya kazi kwa kujitegemea bila kutegemea wasaidizi, akitoa mfano wa watu waliopata mafunzo na sasa wanaweza kwenda kazini na kutekeleza majukumu yao wenyewe.

Amesema Internet Governance ina uhusiano mkubwa na digital inclusion, kwa kuwa usimamizi mzuri wa mtandao unapaswa kuhakikisha makundi yote katika jamii, wakiwemo watu wenye mahitaji maalum, yanapata fursa sawa za kutumia teknolojia na kunufaika na uchumi wa kidijitali.

Aidha, amesema kuna umuhimu wa kuandaa mfumo maalum wa kuwajengea uwezo watu wenye ulemavu, ikiwamo kuwafundisha viziwi kupitia viziwi wenzao na wasioona kupitia wasioona wenzao, hasa katika matumizi ya teknolojia na ujuzi wa kujiajiri.

Amesema hatua hiyo inaweza kusaidia kutatua changamoto zinazotokana na upungufu wa walimu wenye uwezo wa kutumia lugha na mbinu zinazofaa kuwafundisha watu wenye mahitaji maalum, huku ikiongeza idadi ya watu wenye ulemavu wanaoweza kuingia katika sekta za TEHAMA.

Kwa upande wake, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, College of ICT, Dkt.Joseph Mushi amesema chuo hicho kinashirikiana na Tanzania Internet Governance Chapter kuwawezesha vijana kupata ujuzi unaoendana na mahitaji ya dunia ya sasa, ikiwamo kupitia mafunzo na uboreshaji wa mitaala.

Amesema UDSM imekuwa ikifanya mapping kati ya mahitaji yanayotokana na sekta ya TEHAMA na yale yanayojadiliwa kupitia Internet Governance, ili kuhakikisha wahitimu wanakuwa na ujuzi unaoendana na mahitaji ya soko la ajira na fursa za kidijitali.

Naye Mkurugenzi wa Internet Society Tanzania Chapter, Dkt. Nazarius Kirama, amesema Tanzania School of Internet Governance inalenga kuwawezesha wananchi kutoka makundi mbalimbali kuelewa kuwa usimamizi wa Internet si jukumu la mtu mmoja, bali ni suala linalohitaji ushiriki wa Serikali, sekta binafsi, mashirika yasiyo ya kiserikali, wataalamu, vyuo na wananchi.

Amesema elimu ya kidijitali inapaswa kupewa kipaumbele ili wananchi waweze kutumia Internet kama fursa ya elimu, ajira na ujasiriamali, huku akitoa wito kwa Serikali na wadau wengine kushirikiana kuhakikisha digital inclusion inafikiwa katika maeneo yote nchini.


Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewataka wananchi wa Kizimkazi na maeneo jirani kutunza na kulinda miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali, akisisitiza kuwa miradi hiyo ni msingi wa uchumi na ustawi wa wananchi wa sasa na vizazi vijavyo.

Rais Samia ametoa kauli hiyo leo Alhamisi, Agosti 13, 2026, Zanzibar, mara baada ya kuzindua Mradi wa Maji Kizimkazi, ambapo amesema uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali kupitia miradi mbalimbali unapaswa kulindwa ili iendelee kutoa huduma na manufaa yaliyokusudiwa kwa muda mrefu.

“Ni wajibu na ni lazima tutunze miradi hii kama tunavyotunza macho yetu. Miradi hii ni fursa zetu, ni uchumi na ustawi wa maisha yetu,” amesema Rais Samia.

Amesema mafanikio ya utekelezaji wa miradi hiyo yanatokana kwa kiasi kikubwa na uwepo wa amani nchini, hivyo amewataka wananchi kuendelea kuitunza amani ili Serikali iweze kuendelea kutekeleza miradi ya maendeleo na kuboresha maisha yao.

“Miradi hii tumeweka kuileta kwa sababu nchi yetu ina amani. Niombe sana ndugu zangu tuendelee kutunza amani yetu ili tupate maendeleo zaidi,” amesema.

Rais Samia pia amesema kaulimbiu ya “Mapinduzi Daima” inapaswa kuendelea kuakisi mapinduzi katika maendeleo na kuboresha maisha ya wananchi, akieleza kuwa Mapinduzi yalishafanyika na jukumu la sasa ni kuhakikisha mafanikio hayo yanaendelezwa kupitia maendeleo endelevu.

“Tunaposema Mapinduzi Daima, Mapinduzi ya sasa ni maendeleo,” amesema.

Akizungumzia Mradi wa Maji Kizimkazi, Rais Samia amesema mradi huo umejengwa kwa kuzingatia mahitaji ya sasa pamoja na ongezeko la watu na ukuaji wa miji, huku uwezo wake ukiwekwa karibu mara mbili ya mahitaji ya sasa ili kuhakikisha wananchi wanaendelea kupata huduma ya maji hata katika miaka ijayo.

Amesisitiza kuwa wananchi wanapaswa kuupenda, kuutunza na kuilinda miundombinu ya mradi huo kwa kuwa fedha nyingi zimetumika katika utekelezaji wake, hivyo uharibifu au matumizi yasiyo sahihi yanaweza kupunguza au kudhoofisha manufaa yanayotarajiwa.

Rais Samia amesema utunzaji wa miradi ya maendeleo ni jukumu la pamoja kati ya Serikali na wananchi, akisisitiza kuwa kulinda miundombinu hiyo ni kulinda uwekezaji unaolenga kuboresha maisha ya wananchi na kuhakikisha huduma hizo zinaendelea kunufaisha jamii kwa sasa na vizazi vijavyo.




Na Mwandishi Wetu
MAMLAKA ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) imepongezwa kwa kuendelea kuboresha utoaji wa mafunzo katika vyuo vyake kote nchini, ikiwemo kuimarisha mitaala inayozingatia mahitaji ya soko la ajira.

Pongezi hizo zimetolewa na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Wanu Hafidh Ameir, alipotembelea banda la VETA Agosti 12, 2026, katika Tamasha la Kizimkazi lililofanyika Dimbani, Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar.

Wanu alisema VETA imeendelea kufanya vizuri katika kuboresha mazingira ya utoaji wa mafunzo ya ufundi, pamoja na kuhuisha mitaala ili iendane na mahitaji ya soko la ajira.

“Nawapongeza kwa kuendelea kuboresha hali ya utoaji mafunzo ya ufundi katika vyuo, hali ya uboreshaji wa mitaala yenye kuendana na mahitaji ya soko la ajira, lakini pia kutoa mafunzo kwa makundi mbalimbali katika jamii yetu. Kundi la wanawake na vijana linaendelea kunufaika na mafunzo haya,” alisema Wanu

Kwa upande wake, Meneja wa VETA Kanda ya Kaskazini, Monica Mbelle, alisema Mamlaka hiyo inaendelea kutoa mafunzo yanayozingatia mahitaji halisi ya soko la ajira, hatua inayolenga kuwawezesha wahitimu kuajiriwa, kujiajiri na kuajiri wengine.

VETA inashiriki katika Tamasha la Kizimkazi lenye kaulimbiu “Kizimkazi Kumenoga, Shangwe na Fursa,” ambalo ufunguzi wake rasmi ulifanyika Agosti 12, 2026, huku kilele cha tamasha hilo kikitarajiwa kufanyika Agosti 14, 2026.

Mamlaka hiyo imeendelea kuwaalika wananchi kutembelea banda lake katika viwanja vya Dimbani, kupata taarifa kuhusu fursa za mafunzo ya ufundi stadi, kuona bidhaa mbalimbali za ubunifu pamoja na kupata huduma za ufundi wa simu za mkononi.
 





Na Mwandishi Wetu.
MAMLAKA ya Mapato Tanzania imeendelea kutoa mafunzo kuhusu mabadiliko ya sheria za kodi kwa mwaka wa fedha 2026/2027, yaliyoanza kutekelezwa Julai 1, 2026 yakilenga kuwawezesha mawakala, wadau wa forodha na watumishi wa mamlaka kuelewa misamaha na taratibu mpya za kodi pamoja na kupanua wigo wa biashara nchini.

Akifungua mafunzo hayo Mkoani Kagera Meneja wa TRA mkoani humo Joseph Mtalemwa amesema utekelezaji wa sheria hiyo unatarajiwa kukuza biashara hususani wawekezaji waliokuwa wakisubiri kupata misamaha ya kodi.

Amesema mafunzo hayo yatafanyika katika maeneo muhimu ya biashara na mipakani ikiwemo Mutukula, Rusumo, Kabanga na Bandari ya Bukoba.
Kwa upande wao, wawezeshaji wa mafunzo hayo Hassan Minga ambaye ni Afisa Mfawidhi wa Forodha Mkoa wa Dodoma na Allan Maduhu afisa Forodha mkuu wamesema baadhi ya mabadiliko hayo yanahusu misamaha kwenye vifaa vya kuchajia vyombo vya moto vinavyotumia nishati ya umeme ili kukuza matumizi ya nishati safi, pamoja na sekta ya uvuvi, ambapo kuna msamaha wa kodi kwenye nyuzi zinazotumika kuzalisha nyavu za kuvulia samaki.

Baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo Marco Gabriel ambaye ni Mwenyeki wa Chama cha Mawakala wa Forodha mpakani Mutukula na Godwin Idan wamepongeza TRA mpango wake wa kutoa elimu ya mabadiliko ya sheria za kodi kwa wadau wote kwani inawasaidia wafanyabiashara kuelewa mabadiliko ya sheria na kutekeleza wajibu wao kwa usahihi, na kusaidia katika ukusanyaji wa mapato ya Serikali kwa pamoja.


Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Shirikisho la Ujerumani zimekubaliana kuendelea na kuimarisha ushirikiano katika sekta mbalimbali za kimkakati, ikiwemo biashara na uwekezaji, afya, mazingira, maji, uchumi wa buluu, ujenzi wa miundombinu, teknolojia na utawala bora, kwa manufaa ya wananchi wa pande zote mbili.

Hayo yamejili leo, Agosti 13, 2026, jijini Dodoma wakati wa mazungumzo kati ya viongozi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na ujumbe kutoka Ujerumani. 

Kwa upande wa Tanzania yameongozwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Dkt. Mahmoud Thabit Kombo, na Katibu Mkuu Balozi Dkt. Samwel Shelukindo huku kwa upande wa Ujerumani yakiongozwa na Mkuu wa Kitengo kinachoshughulikia masuala ya Afrika katika Wizara ya Ushirikiano wa Kiuchumi na Maendeleo Mhe. Joachim Schmitt. 

Akizungumza na ujumbe huo, Waziri Dkt. Kombo na Katibu Mkuu Balozi Dkt. Shelukindo wamepongeza mchango wa Ujerumani katika shughuli mbalimbali za maendeleo nchini Tanzania, huku wakisisitiza utayari wa Serikali ya Tanzania kuendelea kushirikiana na Ujerumani katika kuimarisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii ili kuboresha ustawi wa wananchi.

Kwa upande wake, Mhe. Schmitt amesema Ujerumani inaendelea kuiona Tanzania kuwa mshirika muhimu wa maendeleo barani Afrika na imedhamiria kuimarisha zaidi ushirikiano kati ya nchi hizo mbili. Ameeleza kuwa Serikali ya Ujerumani iko tayari kutazama maeneo mapya ya ushirikiano yanayoendana na mahitaji na fursa zilizopo, ikiwemo teknolojia, ulinzi na usalama pamoja na uchumi wa kidijitali.

Ujerumani ni miongoni mwa nchi kumi zinazoongoza kwa uwekezaji wa kigeni nchini Tanzania. Kwa mujibu wa takwimu za Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA), kufikia Oktoba 2025, miradi 187 ya uwekezaji kutoka Ujerumani ilikuwa imesajiliwa nchini, ikiwa na thamani ya Dola za Marekani milioni 535.63 na kutoa fursa za ajira taktribani 16,427 katika sekta mbalimbali za uchumi.

Ushirikiano huo unaakisi uhusiano wa muda mrefu na unaoendelea kukua kati ya Tanzania na Ujerumani, huku pande zote zikilenga kuutumia kama msingi wa kukuza biashara na uwekezaji, kuhamasisha maendeleo endelevu na kuongeza fursa za kiuchumi na kijamii kwa wananchi.













Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea mfano wa ufunguo wa gari la wagonjwa kutoka kwa Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani, Kanda ya Afrika, Dkt. Ndoungou Salla Ba, wakati wa ziara fupi ya Rais Dkt. Samia katika Kituo cha Afya Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja tarehe 13 Agosti, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizindua Mradi wa Maji Kizimkazi katika moja ya matukio kuelekea kilele cha Tamasha la Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja tarehe 13 Agosti, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akivuta kitambaa kama ishara ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa Skuli ya Sekondari ya Amali Kizimkazi katika moja ya matukio kuelekea kilele cha Tamasha la Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja tarehe 13 Agosti, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na wananchi wa Kizimkazi baada ya kuzindua Mradi wa Maji Kizimkazi katika moja ya matukio kuelekea kilele cha Tamasha la Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja tarehe 13 Agosti, 2026.



Eneo la hifadhi ya Ngorongoro limetajwa kuwa ndio kivutio namba moja kilichotembelewa zaidi na watalii kwa mwaka 2025 ambapo watalii 859,933 walitembelea hifadhi hiyo ambayo ni kivutio namba moja cha utalii barani afrika.

Kwa mujibu wa ripoti ya Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) iliyofanya  utafiti wa wageni wa kimataifa wakati wa kuondoka  mwaka 2025 (The 2025 International visitors Exit Survey report) inaOnyesha kuwa eneo la hifadhi ya Ngorongoro limetembelewa na asilimia 14.2 ya wageni waliowasili chini kwa mwaka huo na kuwa kinara katika maeneo yote ya utalii nchini.

Ongezeko la idadi ya wageni katika hifadhi ya Ngorongoro na maeneo mengine ya nchi inatokana na jitihada za serikali na wadau wa utalii kuendelea kuitangaza Tanzania katika majukwaa na maonesho ya kimataifa huku Ngorongoro ikiboresha huduma za wageni na kuimarisha miundombinu ya utalii kwenye vivutio vilivyopo ndani ya hifadhi ili kuongeza mtawanyiko wa wageni kwenye vivutio hivyo.

Eneo la hifadhi ya Ngorongoro lina vivutio mbalimbali ikiwemo kreta tatu za Ngorongoro, Olmot na Empakai, Vivutio vingine ni pamoja na mazalia ya nyumbu ndutu, mchanga unaohama, maporomoko ya maji endoro, mapango ya tembo, mlima Lolmalasin, jabali la nasera, msitu wa nyanda za juu kaskazini, makumbusho ya olduvai na nyayo za Laetoli zenye umri wa miaka milioni 3.6 iliyopita.

Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro lililoanzishwa mwaka 1959 lenye ukubwa wa kilomita za mraba 8,292 lina hadhi tatu zinazotambuliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO), ambazo ni; Man and Biosphere Reserve (Hifadhi ya Binadamu na Baiolojia), Mixed World Heritage Site (Urithi wa dunia Mchanganyiko), Ngorongoro Lengai UNESCO Global Geopark (Hifadhi ya Jiolojia ya Dunia), Aidha, mwaka 2023 na 2025, Hifadhi ya Ngorongoro ilichaguliwa na Mtandao wa World Travel Awards (WTA) kama Kivutio Bora cha Utalii Barani Afrika (Africa’s Leading Tourist Attraction).

 

Wananchi mkoani Mtwara wameishukuru Serikali kwa kuendelea kujenga na kuboresha miundombinu ya huduma za afya, hatua iliyowarahisishia upatikanaji wa huduma hizo bila kulazimika kusafiri umbali mrefu.

Hayo yamejiri, katika siku ya tatu ya ziara ya kikazi ya Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga (Mb), mkoani humo, yenye lengo la kukagua na kuzindua miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali ya Awamu ya Sita.

Wananchi hao wamesema wanapata huduma za afya kwa wakati na kwa urahisi, jambo walilolieleza kuwa limepunguza changamoto ya kufuata matibabu katika maeneo ya mbali.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Waziri Kapinga amesema Serikali inalenga kuboresha huduma za afya ili wananchi wapate matibabu kwa urahisi na kuendelea na shughuli zao za uzalishaji, hivyo kuimarisha uchumi wa familia na Taifa.

Amesema kusogeza huduma za afya karibu na wananchi ni sehemu ya juhudi za Serikali kuhakikisha wananchi wanapata huduma muhimu kwa wakati.

Aidha, amewataka wananchi kuendelea kushirikiana na Serikali katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo, akisisitiza kuwa ushirikiano ni msingi wa maendeleo.

Katika siku ya tatu ya ziara hiyo, Waziri Kapinga ametembelea miradi mbalimbali katika Majimbo ya Nanyamba, Mtwara Mjini na Mtwara Vijijini, ikiwemo kuzindua Kituo cha Afya Msangamkuu, kuzindua mabweni mawili na kutoa taulo za kike kwa wanafunzi wa Shule ya Wasichana Mtwara, kukagua ujenzi wa Shule ya Amali Chikota, pamoja na kutembelea Wodi ya Wazazi katika Hospitali ya Wilaya ya Tandahimba.


Top News