Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo, akizungumza na wananchi waliojitokeza katika Kliniki ya Ardhi iliyofanyika Kata ya Zingiziwa, Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, leo Septemba 17, 2026.

Na Victor Masangu, Kibaha
Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Dkt. Nicas Mawazo amewahimiza wazazi na walezi kuachana na tabia ya kuwatelekeza watoto wao hasa katika suala zima la kuwaendeleza kielimu na badala yake washiriki kikamilifu katika kuwa mstari wa mbele kuchangia maendeleo katika kuboresha sekta ya elimu na sio kubaki nyuma.
Kauli hiyo imetolewa na mstahiki Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha wakati wa mahafali ya 16 shule ya msingi Lulanzi Dkt. Nicas Mawazo ambapo amewahimiza wazazi wanapaswa kuweka misingi imara ya kuchangia elimu kwa ajili ya kuweza kuwasaidia watoto wao wasome katika mazingira mazuri na kutimiza ndoto zao ambazo wamejiwekea.
"Kwanza nimefarijika sana kualikwa katika mahafali haya ya darasa la saba katika shule ya msingi Lulanzi lakini kitu kikubwa ambacho ninawaomba wazazi na walezi ni lazima tushirikiane kwa pamoja katika suala zima la kuweza kuchangia mambo mbali ya kielimu na lengo kubwa ni kwa ajili ya watoto wetu ikiwa sambamba na kuboressha miundombinu ya shule pamoja na ujenzi wa ofisi za walimu,"amebainisha Mstahiki Meya.
Mstahiki Meya huyo amebainisha kwamba lengo lake kubwa ni kuendelea kushirikiana bega kwa bega na wazazi pamoja na walezi kwa lengo la kuleta mabadiliko chanya ya kuboresha elimu katika shule mbali mbali zilizopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha na kuahidi kuendelea kutoa sapoti lengo ikiwa ni kuweka mipango madhubuti ya kukuza elimu na wanafunzi kusoma katika mazingira mazuri.
Kwa upande wake Mkuu wa shule ya msingi Lulanzi Bakari amesema kwamba shule hiyo inakabiliwa na changamoto mbali mbali ikiwemo sula la kukosa uzio pamoja na mahitaji mengine ya msingi hivyo ameimba serikali kuweza kuwasaidia kwa hali na mali ili walimu na wanafunzi waweze kusoma katika mazingira ambayo ni rafiki.
Naye mmoja wa wanafunzi ambao wamehitimu katika shule hiyo Janeth Mwangi akisoma risala kwa niaba ya wanafunzi wenzake amebainisha kwamba shule hiyo tangu ianzishwe mnamo mwaka 2007 imeweza kupata mafanikio makubwa ikiwemo katika kufanya vizuri katika nyanja ya kitaaluma pamoja na uboreshaji wa mazingira ya shule.
"Tangu shule hii ilipoanzishwa mnamo mwaka 2007 imeweza kupiga hatua kubwa sana ikiwemo suala la uboreshaji wa miundombinu ya shule japo tunakabiliwa na uhaba wa fedha kwa ajili ya uendeshaji wa shule, uwepo wa wingi wa wanafunzi upungufu mbali mbali wa vifaa vya taaluma,"amebainisha Mwalimu huyo.
Mahafali ya 16 ya shule hiyo ya msingi ya Lulanzi iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha imeweza kuhudhuliwa na wageni mnbali mbali wakiwemo viongozi mbali mbali wa serikali, viongozi wa chama pamoja na wazazi na walezi kwa lengo la kuweza kushiriki na kujumuika katika mahafali hayo ya darasa la saba.
Kampuni ya Sandaland Fashion Wear Limited imetangaza kuchukua hatua za kisheria dhidi ya kauli iliyotolewa hadharani na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, kuhusu jezi za Timu ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars.
Hatua hiyo imetangazwa kupitia tamko rasmi la kampuni hiyo, baada ya kauli ya Makonda iliyotolewa Septemba 16, 2026 kupitia akaunti yake ya Instagram, ambapo alidai kuwa imeathiri jina, chapa, hadhi na uhalali wa bidhaa za Sandaland katika soko.
Katika ujumbe huo, Makonda alinukuliwa akisema:
“Hii sio jezi ya Taifa Stars, Taifa Stars kwa ubora wake hatuwezi kuwa na jezi za kiwango chini hivi. Acheni kutumia picha za Naibu wangu huku ofisi yangu haina taarifa.”
Ujumbe huo uliambatana na picha ya Naibu Waziri Hamis Mwinjuma, maarufu Mwana FA, akiwa amevalia jezi yenye mchanganyiko wa rangi ya njano, bluu, nyeusi na kijani.
Kwa upande wake, Sandaland imesema kauli hiyo imezua taharuki na sintofahamu, huku ikidai kuwa tayari imesababisha madhara ya kiuchumi na kuathiri hadhi ya kampuni.
Kampuni hiyo imeeleza kuwa ina mkataba halali na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) wa kutengeneza na kusambaza jezi za Taifa Stars, ambazo zimetumika katika mashindano mbalimbali ya timu za taifa za wanaume na wanawake.
Sandaland imeongeza kuwa haitanyamaza na inakusudia kuchukua hatua za kisheria dhidi ya kauli hiyo, ikidai kuwa ilitolewa kwa namna inayoweza kuchafua chapa yake.
Aidha, kampuni hiyo imesisitiza kuwa imejenga jina na heshima yake kwa muda mrefu na imepewa dhamana ya kushughulikia jezi za Taifa Stars.
MKURUGENZI wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai, Kamishna wa Polisi Ramadhani Kingai, amegoma kutoa ushahidi kwa upande wa utetezi wa Mwenyekiti wa Chadema, Tundu Lissu, anayekabiliwa na mashtaka ya uhaini katika Mahakama Kuu Masijala Ndogo Dar es Salaam.
Hatua hiyo imempelekea mshtakiwa Lissu, ambaye anajitetea mwenyewe katika kesi hiyo, kufunga ushahidi wa upande wa utetezi.
Kesi hiyo leo, Septemba 18, 2026, iliitwa mahakamani hapo kwa ajili ya kuendelea na ushahidi wa upande wa utetezi, ambapo DCI Kingai alitarajiwa kutoa ushahidi.
Akizungumza mbele ya Jopo la Majaji linaloongozwa na Jaji Dustun Ndunguru, Lissu amedai amekutana na DCI Kingai, ambaye alikuwa amependekeza awe shahidi wake wa leo, ndani ya chumba cha mahakama na kuzungumza naye kwa kina kuhusu suala la kutoa ushahidi kwa upande wa utetezi.
Amedai kuwa baada ya kumweleza Kingai maeneo ambayo angependa ayatolee ushahidi, shahidi huyo alimweleza kuwa hawezi na hayuko tayari kutoa ushahidi kwa upande wa utetezi.
“Mimi nimemuelewa kama hayuko tayari, siwezi kumlazimisha kutoa ushahidi ambao hayupo tayari kuutoa,” amedai Lissu.
Amedai Kingai amemweleza kuwa yeye yuko upande wa watu wanaoomba na watakaoshangilia endapo atapatikana na hatia, hivyo hayuko tayari kutoa ushahidi kwa niaba yake.
“Yeye yuko upande wa wale wanaoomba na watakaoshangilia nikipatikana na hatia, kwa hiyo amesema hayuko tayari kuja kutoa ushahidi kwa niaba yangu,” amedai Lissu.
Amedai Kingai pia amemweleza kuhusu mashahidi wengine wawili ambao ni Mkuu wa Majeshi, CDF Jacob Nkunda, na Mkuu wa Jeshi la Polisi, IGP Camilius Wambura, ambao pia mahakama iliamuru wapelekewe wito, kuwa nao watakaporejea nchini na kupata wito wa mahakama, msimamo wao utakuwa kama wake.
“Kwamba na wao hawatakuwa tayari kutoa ushahidi kwa upande wa utetezi, hawawezi kwa sababu ile ile ya wale wanaoombea na watakaoshangilia nikipatikana na hatia,” amedai Lissu.
Kutokana na hali hiyo, Lissu amesema hana mashahidi wengine wa kuwaita na hivyo ameomba kufunga ushahidi wa upande wa utetezi.
Baada ya kusikiliza maelezo hayo, kesi hiyo sasa imefungwa kwa pande zote mbili na kuomba kupangiwa siku ya kuwasilisha hoja za mwisho.
Upande wa utetezi umeeleza kuwa ratiba ya kikao cha mahakama inaishia Septemba 25, hivyo kubaki siku saba za kuandaa hoja za mwisho.
Lissu amesema yuko tayari kuwasilisha hoja hizo Jumatano, huku akieleza kuwa mwenendo wa kesi una hoja zaidi ya kurasa 1,000.
Upande wa Jamhuri umekubaliana na Lissu kuhusu tarehe hiyo na kueleza kuwa utakuwa tayari kwa ajili ya kuwasilisha hoja za mwisho.
Kesi imeahirishwa hadi Septemba 23, 2026.
Wakala wa Vipimo (WMA) umewataka wafanyabiashara na wananchi kuacha kutumia madebe, makopo, mafungu na vifaa vingine visivyotambuliwa kisheria kama vipimo katika biashara, ukieleza kuwa matumizi ya vifaa hivyo ni kinyume cha sheria na yanaweza kuchukuliwa kuwa kosa la jinai.
Akizungumza leo jijini Dodoma katika mkutano na waandishi wa habari kuhusu utekelezaji wa majukumu ya Wakala kwa mwaka wa fedha 2025/26 na mwelekeo wa mwaka 2026/27, Afisa Mtendaji Mkuu wa WMA, Alban Kihulla, amesema vipimo visivyo rasmi vinaweza kusababisha bidhaa kupimwa kwa viwango tofauti na hivyo kuwanyima haki watumiaji.
Kihulla amesema matumizi ya madebe na makopo katika kupima bidhaa kwa uzito hayatoi kipimo cha uhakika kwa kuwa kiasi kinachopatikana kinaweza kutofautiana kutoka chombo kimoja hadi kingine, jambo linaloweza kusababisha mfanyabiashara au mlaji kupata kiwango kisicho sahihi cha bidhaa anayolipia.
“Madebe, makopo, visado na mafungu sio vipimo na tumeendelea kutoa elimu kwa wananchi, lakini pia tunaendelea kuchukua hatua dhidi ya wanaojihusisha na upimaji wa aina hiyo,” amesema Kihulla.
Amesema WMA itaendelea kusimamia matumizi ya vipimo sahihi kwa lengo la kuhakikisha biashara zinafanyika kwa haki na kulinda maslahi ya wafanyabiashara pamoja na watumiaji, huku akiwataka wafanyabiashara kuhakikisha wanakuwa na mizani inayokidhi matakwa ya kisheria katika maeneo yao ya biashara.
Aidha, Kihulla amewahimiza wananchi kujenga utamaduni wa kuhakikisha bidhaa wanazonunua zinapimwa kwa mizani sahihi, akisisitiza kuwa matumizi ya vipimo vinavyotambulika kisheria ni sehemu muhimu ya kulinda haki za mlaji na kuhakikisha kila mmoja anapata kiwango cha bidhaa anachostahili.
Wakala wa Vipimo (WMA) umesema jukumu la kuhakikisha vipimo vinavyotumika katika biashara vinafanyika kwa usahihi, pamoja na kutekelezwa kwa mujibu wa sheria, lina msingi pia katika mafundisho yanayopatikana katika vitabu vya dini, ikiwemo Qur’an Tukufu na Biblia Takatifu.
Afisa Mtendaji Mkuu wa WMA, Alban Kihulla, ameyasema hayo leo jijini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu utekelezaji wa majukumu ya Wakala kwa mwaka 2025/26 pamoja na mwelekeo wa utekelezaji kwa mwaka 2026/27.
Kihulla amesema maandiko matakatifu yanasisitiza umuhimu wa kufanya vipimo kwa usahihi, hivyo wafanyabiashara wanapaswa kuhakikisha wanatumia vipimo sahihi na vilivyohakikiwa kwa mujibu wa sheria. Amesema hatua hiyo ni muhimu katika kujenga uadilifu na kuaminiana katika shughuli za biashara.
“Mtu anayetaka kufanya biashara afanye biashara iliyonyooka. Lazima awe na vipimo sahihi na ambavyo vimehakikiwa kwa mujibu wa sheria,” amesema Kihulla.
Amesema WMA, ikiwa ni sehemu ya safari ya kuelekea utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050, itaendelea kuhakikisha vipimo vinavyotumika katika shughuli mbalimbali vinaendana na viwango vinavyotakiwa. “Kilo moja ukipimiwa kweli iwe kilo moja, na si vinginevyo,” amesema.
Kwa mujibu wa Kihulla, usimamizi wa vipimo unalenga kujenga uaminifu katika biashara, kumlinda mlaji pamoja na mtoa huduma, huku ukiisaidia Serikali kupata mapato yanayostahili kupitia matumizi ya vipimo sahihi na vilivyohakikiwa.
Amesema WMA itaendelea kuwa chombo muhimu katika kuwezesha utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050, hususan katika kujenga mazingira ya biashara yenye uaminifu na hatimaye kuchangia ujenzi wa Taifa lenye uchumi imara, jumuishi na wenye ushindani.
NA MWANDISHI WETU, DODOMA
Wananchi na viongozi wa Zanzibar wamepongezwa kwa kufikia muafaka wa kitaifa kwa kuimarisha umoja na mshikamano kuelekea ujenzi wa taifa lenye maendeleo.
Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Taifa na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu (MCC), Mary Chatanda, Septemba 18, 2026, Jijini Dodoma.
Chatanda amesema, hakuna shaka kuwa, wananchi na viongozi wa Zanzibar, wamesukumwa na dhamira ya dhati ya ujenzi wa taifa lao badala ya kutanguliza tofauti zao za kisiasa na maslahi binafsi.
"Niwapongeze wananchi na viongozi wa Zanzibar ambao waliangalia maendeleo badala ya tofauti zao za vyama, waliangalia Zanzibar waitakayo yenye neema na ustawi badala ya misuguano isiyokwisha, ndiyo maana wakaona wakae pamoja, waelewane ili kuunganisha nguvu ya pamoja katika kusukuma mbele gurudumu la maendeleo," amesema Chatanda.
Aidha, Chatanda amempongeza Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Dkt. Hussein Mwinyi kwa kuwa na hekima, busara na utulivu huku akiwashirikisha kikamilifu viongozi wastaafu na wengine kutoka vyama vya upinzani katika kutafuta muafaka wa pamoja ili Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK) iundwe na kufanya kazi.
"Rais Dkt. Hussein Mwinyi ameonyesha ukomavu mkubwa wa kiuongozi, kwa kweli nampongeza sana. Vilevile, niwapongeze wanasiasa hasa kutoka Chama cha ACT- Wazalendo, kwa kukubali kukaa meza moja ya mazungumzo ili muafaka upatikane, hatimaye Zanzibar isonge mbele kimaendeleo. Kwa kweli Wazanzibar wamethibitisha kuwa inawezekana kufikia muafaka wa kitaifa kupitia meza ya mazungumzo," amesema.
Ikumbukwe kuwa, tangu kumalizika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 2025, kumekuwa na mazungumzo ya pamoja yanayoendelea ili kukamilisha uundwaji wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa baina ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na ACT - Wazalendo.
Septemba 17, 2026, Kamati ya Uongozi ya ACT- Wazalendo, ilikaa kikao maalum kilichofanyika ofisi ndogo za Chama hicho, Vuga Mjini Unguja, ambapo pamoja na mambo mengine, kilifanya uteuzi wa jina la mwanachama anayependekezwa kuwa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar.
Kufuatia kikao hicho, Septemba 18, 2026, Rais Dkt. Hussein Mwinyi, alifanya uteuzi wa Othman Masoud Othman, kuwa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, ambapo ataapishwa rasmi Septemba 22, 2026, Ikulu, Zanzibar.
Kukamilika kwa mchakato wa upatikanaji wa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, kunaendeleza mchakato wa kuteua mawaziri kutoka ACT- Wazalendo ili kukamilisha uundwaji wa serikali ya pamoja ambayo itakuwa chachu ya kuendeleza mipango mizuri ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi wa Zanzibar huku umoja, amani, upendo na mshikamano ukiwa nguzo kuu ya maendeleo hayo.
Mbunge wa viti maalumu Mkoa wa Pwani kupitia chama cha mapoinduzi (CCM) Mariamu Ulega katika kuunga mkono juhudi za seriklai katika kuboresha sekta ya elimu ameahidi kuchangia kiasi cha shilingi milioni 2 kwa ajili ya kuboresha miundombinu katika shule ya msingi ya Mkoani B iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha hususan katika suala la ujenzi wa kujenga uzio.
Akizungumza wakati wa mahafali ya kwanza kwa mchepua wa kiingereza katika shule ya msingi Mkoani B Katibu wa Jumuiya ya umoja wa wanawake (UWT) Mkoa wa Pwani Aziza Hussein kwa niaba ya mgeni rasmi Mbunge wa viti maalumu Mariamu Ulega ambaye pia Mke wa Waziri wa Ujenzi Abdalah Ulega.
Katibu huyo huyo wa UWT Mkoa akitoa salamu za Mbunge huyo amebainisha kwamba anatambua umuhimu mkubwa wa suala zima la elimu hivyo ameamua kuchangia kiasi hicho cha shilingi milioni 2 ambazo zitaweza kusaidia katika mwendelezo wa ujenzi wa uzio katika shule hiyo ya msingi Mkoani B yenye mchepuo wa kiingereza.
"Nashukuru sana nimeweza kushiriki na kualikwa katika mahafali haya ya kwanza katika shule hii ya msingi mkoani B lakini mimi ni Katibu wa UWT Mkoa wa Pwani lakini kwa leo nimepewa heshima ya kipekee kwa ajili ya kuweza kumwakilisha Mbunge wa viti maalumu mheshimiwa Mariamu Ulega ambaye yeye ndiye aliyetakiwa kuwa mgeni rasmi katika sherehe hizi z amahafali,"amebainisha Katibu huyo.
Aidha katibu huyo ameongeza kwamba lengo kubwa ni kuendelea kushirikiana bega kwa bega na walimu, wazazi pamoja na wadau mbali mbali wa maendeleo katika kutoa sapoti na michango yao ambayo itaweza kusaidia katika kukuza sekta ya elimu sambamba na kuboresha zaidi miundombinu katika shule hiyo.
"Mbunge wenu wa viti maalumu mheshimiwa Mariam Ulega ameniagiza kuja kumwakilisha na amesema yupo pamoja nanyi na kwamba amesema kuwa anachangia kiasi cha shilingi milioni mbili na na kuelekeza kwamba fedha hizo zitumike katika kuboresha miundombinu ya ujenzi wa uzio ili watoto hao waweze kusoma katika mazingira ambayo ni rafiki na salama na kwamba ataendelea kuisaidia shule hiyo katika mambo mengine mbali mbali,"ameongeza Katibu huyo.
Katika hatua nyingine amempongeza kwa dhati Rais wa awamu ya sita Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuweza kutenga fedha nyingi ambazo zimeweza kuleta mabadiliko makubwa katika kutekelza miradi ya maendeleo hususan kuboresha sekta ya elimu ikiwemo ujenzi i wa madarasa pamoja na madawati.
Pia katibu huyo mbali na kutoa salamu za mheshimiwa Mbunge wa viti maalumu Mariamu Ulega amesema na wao kama uongozi wa UWT Mkoa wa Pwani wameamua kuchangia kiasi cha shilingi laki tano ikiwa ni moja na jitihada za kuunga mkono juhudi ambazo zinafanywa na Rais Dkt Samia Suluhu Hassan katika kuboresha sekta ya elimu hapa nchini.
Nao baadhi ya wazazi na walezi akiwemo Teodory Joseph pamoja na Joseph Ogutu wameipongeza serikali kwa kuweza kuboresha sekta ya elimu huku wakiiomba kuweka misingi madhubuti ya kuendelea kutenga shule nyingine na kuziingiza katika progamu hiyo ya kuwa na mchepuo wa masomo ya kiingereza.
Mahafali ya kwanza ya kwa mchepuo wa kiingereza katika shule ya Msingi Mkoani B iliyopo Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Mkoa wa Pwani imeweza kuhudhuliwa na viongozi mbali mbali wa serikali, wazazi na walezi pamoja na wadau wengine mbali mbali wa maendeleo katika sekta ya elimu.
Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Paul Christian Makonda, ametangaza kutoutambua mchakato wa kubadilisha jezi za timu za taifa, akisema umefanyika bila kuishirikisha Wizara licha ya maelekezo aliyoyatoa Februari 2026.
Sambamba na hatua hiyo, Waziri Makonda ameagiza kuundwa kwa kamati maalumu itakayochunguza mikataba ya wazabuni wa jezi hizo, manufaa yake kwa timu za taifa pamoja na mapato yatokanayo na mauzo ya jezi.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Wizara hiyo leo, Septemba 18, 2026, uchunguzi huo unalenga kubaini iwapo mikataba iliyopo inanufaisha timu za taifa kwa kiwango kinacholingana na fedha nyingi zinazotolewa na Serikali kugharamia timu hizo.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa Februari 2026, Waziri Makonda alitoa maelekezo ya kuboresha jezi za timu za taifa ili ziakisi utambulisho wa Tanzania na kuzalisha manufaa mapana zaidi kwa nchi.
Hatua hiyo inatajwa kuwa muhimu kutokana na uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali katika maandalizi ya timu za taifa zinazoshiriki mashindano ya kimataifa, pamoja na maandalizi ya Tanzania kuwa mwenyeji mwenza wa mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika mwaka 2027 (AFCON 2027).
Wizara imebainisha kuwa jezi za timu za taifa hazipaswi kuangaliwa kama mavazi ya wachezaji pekee, bali pia kama sehemu ya utambulisho wa taifa na chanzo cha mapato yanayoweza kusaidia uendeshaji wa timu hizo.
“Pamoja na kutoutambua utambulisho wa jezi za timu ya taifa, Waziri Makonda ataunda Kamati ya kuchunguza mikataba ya mzabuni wa jezi hizo, ili kubaini manufaa ya mikataba hiyo kwa timu za taifa ambazo zimekuwa zikigharimiwa na Serikali kwa fedha nyingi,” imeeleza sehemu ya taarifa hiyo iliyosainiwa na Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Bi Zaituni Mkwama.
Kamati hiyo pia itachunguza namna mapato yanayotokana na mauzo ya jezi za timu za taifa yanavyokusanywa na mchango wake katika kugharamia shughuli za timu hizo.




.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)





.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)


.jpeg)


