Na Mwandishi Wetu, Tanga
CHUO cha Kodi (ITA) kimeshiriki Maonesho ya Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanayoendelea katika Viwanja vya Usagara jijini Tanga, kwa kutoa elimu kuhusu majukumu ya Chuo hicho pamoja na fursa za mafunzo zinazotolewa.

Wanafunzi na wadau mbalimbali waliotembelea banda la ITA wamepata fursa ya kufahamu kwa kina kuhusu programu za mafunzo zinazotolewa na Chuo hicho, huku wakihamasishwa kujiunga na mafunzo hayo.

Maonesho hayo yaliyoanza Agosti 15, 2026, yamekuwa pia jukwaa kwa ITA kuwaelimisha wananchi kuhusu nafasi ya taaluma mbalimbali katika Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na maeneo mengine ya ajira.

Akizungumza na wanafunzi waliotembelea banda hilo, Afisa Mkuu wa Uhusiano wa Umma wa ITA, Oliver Njunwa, amesema mwanafunzi anayelenga kufanya kazi TRA anapaswa kuzingatia masomo yote kwa kuwa Mamlaka hiyo inaajiri wataalamu wenye taaluma mbalimbali.

“TRA ina wafanyakazi wenye taaluma mbalimbali, hivyo mwanafunzi anatakiwa kuzingatia masomo yote na kufanya vizuri katika masomo yake,” amesema Njunwa.

Aidha, amewataka wanafunzi wanaotaka kusoma ITA kutokuwa na mtazamo wa kwamba mhitimu wa Chuo hicho anapaswa kufanya kazi TRA pekee, bali kuwa tayari kufanya kazi katika taasisi au maeneo mengine ambako taaluma zao zinahitajika.

“Mwanafunzi aliyesoma ITA anajengwa kufanya kazi sehemu yoyote ambayo taaluma aliyoisomea inahitajika pamoja na kujiajiri,” amesema.

Maonesho ya Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanaendelea katika Viwanja vya Usagara jijini Tanga hadi Agosti 24, 2026.

Dar es Salaam.
MFUKO wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) umeendesha mafunzo maalum kwa waandishi wa habari kuhusu masuala ya hifadhi ya jamii, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuongeza uelewa wa umma na wanachama kuhusu huduma, haki na wajibu unaotolewa na Mfuko huo.

Mafunzo hayo ya siku mbili yaliyoanza Agosti 17, 2026, yalifunguliwa na Meneja wa PSSSF Kanda ya Kinondoni, Bw. Costa Mpagike, kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF, Bw. Fortunatus Magambo.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Bw. Mpagike alisema lengo kuu ni kujenga na kuimarisha uhusiano wa kudumu kati ya PSSSF na vyombo vya habari ili kuwezesha utoaji wa taarifa sahihi kwa umma kuhusu masuala ya hifadhi ya jamii.

“Kama mjuavyo, mafunzo haya ya siku mbili yanalenga kujenga na kuimarisha uhusiano wa kudumu na vyombo vya habari pamoja na waandishi wa habari, kuongeza uelewa wa umma na wanachama kuhusu shughuli za PSSSF, haki na wajibu wao kupitia mada mbalimbali za mafunzo, uzalishaji wa makala za uchambuzi na kupunguza upotoshaji wa taarifa” alisema Bw. Mpagike.

Aliongeza kuwa mbali na kuwapatia maarifa kuhusu mifumo na huduma za PSSSF, Mfuko unatamani washiriki wa mafunzo hayo wawe mabalozi wa kueneza taarifa sahihi za hifadhi ya jamii katika vyumba vya habari na kwenye jamii kwa ujumla.

“Tutawajengea uwezo ili muwe na taarifa sahihi kuhusu PSSSF na huduma zake, jambo ambalo litawarahisishia kuandika habari kwa ukweli, weledi na usahihi zaidi,” alisisitiza.

Baadhi ya washiriki walieleza kufurahishwa na fursa hiyo ya mafunzo, wakisema elimu waliyoipata itawasaidia kuboresha kazi zao za uandishi wa habari, hususan katika kuripoti masuala ya hifadhi ya jamii.

Mratibu wa mafunzo hayo, Bw. Nevile Meena, amesema elimu waliyoipata iwasaidie katika shughuli zao za uandishi wa habari.

“ Kama hujui kitu huwezi kuandika kwa usahihi, kama unafahamu jambo utaandika kwa usahihi, nawashukuru PSSSF kwa kutujengea uelewa, mimi binafsi nimekuwa mwandihi wa habari wa siku nyingi lakini kuna vitu vingine nimevifahamu sasa kujifunza hakuna mwisho. Naamini tutayatendea haki haya mafunzo na tutafanya vizuri katika kazi zetu.” Amesisitiza Bw. Meena

Mwandishi wa habari kutoka Kampuni ya Magazeti ya Serikali (TSN), Bi. Zena Chande, alisema mafunzo hayo yamemsaidia kuongeza uelewa kuhusu huduma na mafao yanayotolewa na PSSSF.

“Kimsingi nimeongeza uelewa kuhusu namna PSSSF inavyotekeleza majukumu yake. Mambo tuliyojifunza hapa yatanisaidia kufanya kazi yangu kwa ubora zaidi. Kabla ya mafunzo haya sikuwa na uelewa wa kutosha kuhusu kiinua mgongo, pensheni na sifa za kufaidika na mafao hayo, lakini sasa nimeelewa kwa kiwango kikubwa,” alisema Bi. Chande.

“ Ni mafunzo yenye tija kubwa sana kwetu sisi waandishi wa habari ambao tuna nafasi kubwa ya kuwasiliana na jamii wakiwemo wanachama wa PSSSF,” amesema Bi. Julieth Robert, mwandishi wa habari wa ITV.

Kwa upande wake, mwandishi wa habari mkongwe ambaye kwa sasa ni mnufaika wa pensheni kutoka PSSSF, Bw. Beda Msimbe, alitoa ushuhuda kuhusu umuhimu wa pensheni katika maisha ya mstaafu.

“Hii pensheni inanisaidia sana katika maisha yangu ya kila siku. Baada ya kustaafu, changamoto za maisha zipo, lakini mimi ninafurahia kuwa mwanachama wa PSSSF. Sasa ni mstaafu ninayepokea pensheni kila mwezi. Kila inapofika tarehe 22 napokea ujumbe mfupi wa simu unaonijulisha kuwa fedha zimeingizwa kwenye akaunti yangu. Kwa kweli, PSSSF wanatekeleza jukumu lao vizuri,” alisema Bw. Msimbe.

Mafunzo hayo ni sehemu ya mkakati wa PSSSF wa kuendelea kushirikiana na wadau mbalimbali, hususan vyombo vya habari, katika kuelimisha umma kuhusu umuhimu wa hifadhi ya jamii na huduma zinazotolewa na Mfuko huo.





Na Janeth Raphael - MichuziTv


Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 ya kujenga Tanzania yenye uchumi wa kisasa, jamii yenye ustawi, huduma bora za kijamii pamoja na matumizi makubwa ya teknolojia na ubunifu, imeelezwa kuwa inahitaji Serikali za Mitaa imara, zenye uwezo na zinazowajibika ili kuhakikisha malengo hayo yanafikiwa kwa ufanisi na kwa usawa.

Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Dkt. Jafar Seif, amesema ugatuzi wa madaraka katika mamlaka za Serikali za Mitaa ni nyenzo muhimu ya kufanikisha Dira hiyo, kwa kuwa unawawezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika maamuzi na utekelezaji wa shughuli za maendeleo katika maeneo yao.

Dkt. Seif ameyasema hayo leo jijini Dodoma wakati akifungua Mkutano Mkuu wa 16 wa Taasisi ya Maboresho katika Mamlaka za Serikali za Mitaa (TOA), unaofanyika chini ya kaulimbiu isemayo “Ugatuzi wa Madaraka katika Mamlaka za Serikali za Mitaa ni Nyenzo Madhubuti ya Kufikia Dira ya Taifa 2050.”

Amesema ugatuzi wa madaraka si suala la kiutawala pekee, bali ni msingi wa kuwapa wananchi nafasi ya kushiriki katika maamuzi yanayohusu maendeleo yao, akieleza kuwa Serikali za Mitaa ndizo zilizo karibu zaidi na wananchi na zina nafasi kubwa katika kuhakikisha huduma na miradi ya maendeleo inawafikia kwa wakati.

“Serikali za Mitaa zikiwa imara na zenye uwezo wa kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, Taifa linaweza kufikia malengo yake kwa haraka zaidi na kwa usawa,” amesema Dkt. Seif.

Amesema Serikali imepanga kuchukua hatua zaidi katika eneo la ugatuzi wa madaraka kwa kuimarisha mifumo mbalimbali ya kiutendaji na usimamizi, hususan katika eneo la fedha, hatua inayolenga kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa miradi na utoaji wa huduma kwa wananchi.

Dkt. Seif amesema kwa sasa fedha za utekelezaji wa miradi ya maendeleo zinapelekwa moja kwa moja katika taasisi za Serikali zilizopo ngazi za chini, ikiwemo shule, zahanati, ofisi za kata, vijiji pamoja na maeneo mengine ya kiutawala na kiutendaji.

Ameeleza kuwa hatua hiyo inalenga kuhakikisha rasilimali zinazotengwa kwa ajili ya maendeleo zinawafikia walengwa moja kwa moja na kutumika katika kutatua changamoto zinazowakabili wananchi katika maeneo yao.

Aidha, Dkt. Seif amesema ili Dira ya Taifa ya 2050 ifikiwe, Serikali za Mitaa zinapaswa kuimarisha maeneo muhimu ikiwemo uongozi bora na uwajibikaji, mipango madhubuti ya maendeleo, usimamizi wa rasilimali za umma, ushirikishwaji wa wananchi pamoja na matumizi ya TEHAMA katika utoaji wa huduma.

Amesema TOA imeendelea kuwa jukwaa muhimu la kuwakutanisha viongozi na wataalamu wa Serikali za Mitaa kwa ajili ya kubadilishana uzoefu, kujifunza na kutafuta suluhisho la changamoto zinazojitokeza katika ngazi za chini za utendaji.

Dkt. Seif amesisitiza kuwa mafanikio ya ugatuzi wa madaraka yanategemea kwa kiasi kikubwa uwezo wa taasisi kujenga mazingira ya uwazi, uwajibikaji na ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu ya Serikali za Mitaa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TOA, Albert Msovela, amesema taasisi hiyo itaendelea kushirikiana na Serikali katika kusimamia maendeleo ya wananchi na kuimarisha utawala bora, huku akisisitiza umuhimu wa kuendelea kujenga uwezo wa mamlaka za Serikali za Mitaa ili ziweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.

Mkutano huo wa 16 wa TOA unajadili masuala mbalimbali yanayohusu maboresho ya utendaji wa Serikali za Mitaa, ugatuzi wa madaraka na namna ya kuimarisha utoaji wa huduma kwa wananchi katika kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050.






Na  Avila Kakingo
SERIKALI imewataka wamiliki na waendeshaji wa miundombinu muhimu ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kukamilisha usajili wake ndani ya miezi sita, huku ikisisitiza kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kuilinda dhidi ya mashambulizi ya mtandao, hitilafu na majanga.

Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Angellah Kairuki, amesema usajili huo unalenga kuiwezesha Serikali kutambua miundombinu yenye umuhimu mkubwa kwa usalama, uchumi na ustawi wa jamii na kuhakikisha inalindwa dhidi ya vitisho vinavyoweza kuvuruga huduma muhimu.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumatano, Agosti 19, 2026, jijini Dar es Salaam, Kairuki amesema wamiliki na waendeshaji wanatakiwa kukamilisha usajili huo ifikapo Desemba 19, 2026.

Amesema miundombinu muhimu ya TEHAMA inahusisha mali, vifaa, mifumo ya kompyuta na mitandao inayoshikika na isiyoshikika ambayo endapo itashindwa kufanya kazi inaweza kusababisha madhara makubwa kwa usalama, uchumi na jamii.

Amesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha miundombinu hiyo inaendelea kuwa salama, inapatikana na kufanya kazi kwa uhakika hata wakati wa mashambulizi ya mtandao, hitilafu za kiufundi au majanga.

Kwa mujibu wa Kairuki, sekta zenye miundombinu hiyo ni pamoja na habari na mawasiliano, fedha na benki, maji, afya, nishati, madini, usafirishaji, chakula na kilimo, ujenzi, uchumi wa buluu, mazingira, viwanda, ulinzi, anga, elimu, utawala wa kiraia, ulinzi wa raia, ardhi pamoja na usalama na utulivu wa umma.

Amesema hatua hiyo inatekelezwa kwa mujibu wa Sheria ya Makosa ya Mtandao Namba 14 ya mwaka 2015, hususan Kifungu cha 28(1), kinachompa Waziri mwenye dhamana ya mawasiliano mamlaka ya kutangaza miundombinu muhimu ya TEHAMA.

“Ni lazima kwanza itambuliwe kwa kuzingatia vigezo vilivyowekwa kisheria. Ulinzi wa miundombinu hiyo unalenga kuhakikisha inabaki salama, inapatikana na inafanya kazi kwa uhakika hata wakati kunapotokea mashambulizi ya mtandao, hitilafu au majanga,” amesema.

Kairuki amesema uharibifu wa miundombinu hiyo unaweza kusababisha madhara makubwa ya kiusalama na kiuchumi na kwamba sheria imeweka adhabu kwa mtu atakayebainika kufanya uharibifu huo.

Amesema kwa mujibu wa Kifungu cha 29 cha Sheria ya Makosa ya Mtandao ya mwaka 2015, mhusika anaweza kutozwa faini isiyopungua Sh100 milioni au mara tatu ya hasara iliyosababishwa, kifungo kisichopungua miaka mitano au adhabu zote kwa pamoja.

Amesema Serikali imeandaa miongozo mitano itakayowawezesha wamiliki na waendeshaji wa miundombinu muhimu ya TEHAMA kuelewa wajibu wao katika kuitambua, kuisimamia na kuilinda.

Miongozo hiyo inahusu utambuzi na usimamizi wa miundombinu muhimu ya TEHAMA, ukaguzi, tathmini ya hatari, uadilifu na uhalisia wa data pamoja na mipango ya urejeshaji wa huduma baada ya janga.

Amesema wamiliki na waendeshaji wa miundombinu hiyo wanapaswa kutumia mfumo maalumu wa CII Portal kwa ajili ya usajili na kuwasilisha taarifa zinazohitajika kwa mujibu wa taratibu zilizowekwa.

Aidha, Kairuki amesema changamoto za kiusalama zinazohusisha miundombinu muhimu ya TEHAMA zinapaswa kuripotiwa kwa mamlaka husika ndani ya saa 24 tangu kubainika kwake.

Akizungumza na Mwananchi, Mkurugenzi wa Mawasiliano, Munaku Mulemwa, amesema usajili huo ni hatua muhimu katika kujenga mazingira salama na imara ya kidijitali yatakayowezesha huduma muhimu kuendelea kutolewa kwa ufanisi licha ya kuongezeka kwa vitisho vya usalama wa mtandao.

Amesema usajili utaiwezesha Serikali kuwa na uelewa wa miundombinu inayohitaji ulinzi maalumu, kutathmini vihatarishi vinavyoweza kuiathiri na kuweka mazingira bora ya kuilinda dhidi ya vitisho vinavyoendelea kuongezeka.

“Hatua hii inasaidia sana kutambua miundombinu hiyo, kutathmini vihatarishi vinavyoweza kuiathiri na kuweka mazingira bora ya kuilinda dhidi ya vitisho vinavyoendelea kuongezeka katika ulimwengu wa sasa,” amesema Mulemwa.







Na George Maziku, Mbogwe

WACHIMBAJI wadogo katika mgodi wa dhahabu wa Mwinula Group Gold Rush uliopo kijiji cha Mgaya, kata ya Lugunga, wilayani Mbogwe, mkoa wa Geita wamemuomba Rais Samia Suluhu Hassan kuwasaidia kupata umeme katika mgodi wao ili kuwarahisishia kazi ya uchimbaji na uchenjuaji dhahabu.

Wachimbaji hao wametoa kilio chao mbele ya waandishi wa vyombo mbalimbali vya habari waliotembelea mgodi huo Jumatatu, Agosti 10, mwaka huu.

Akizungumzia adha wanayopata kutokana na ukosefu wa umeme mgodini hapo, katibu mkuu wa mgodi huo Jesto Shashu alisema wamekuwa wakitumia gharama kubwa katika uchimbaji na uchenjuaji kutokakana na matumizi ya nishati ya mafuta ambayo kwa sasa yamepanda bei, hali inayowasababishia hasara kubwa.

“Hali ya kukosa umeme pia imesababisha mgodi wetu kukikmbiwa na wawekezaji, kama ambavyo mnaona wenyewe ndugu waandishi idadi ya duara zinazofanya kazi ni ndogo sana baada ya wawekezaji wengine kutelekeza duara zao na kuondoka kutokana na kulemewa na gharama za uchimbaji”, alibainisha Shashu.

Mgodi huo ulioanza miaka mitatu iliyopita kwa sasa umeshuka katika uzalishaji, hali ambayo imewalazimisha watu wengi wanaonufaika na uchimbaji, wakiwemo wachimbaji, wabeba mizigo ya mawe, bodaboda, mamalishe, wafanyabiashara mbalimbali, kukimbilia migodi mingine ambayo uzalishaji upo juu.

Katibu huyo amesema kuwa mgodi wake una uwezo mkubwa wa kuzalisha ikiwa utapatiwa umeme, na kuzidi kumlilia Rais Samia kuwaelekeza wasaidizi wake kupeleka umeme kwa haraka katika mgodi huo.

“Mwamba wa dhahabu uliopo kwenye mgodi wetu ni mkali sana, na kama serikali ya mama yetu Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ikitupatia umeme mwaka huu, tunaweza kuwa mgodi mkubwa sana ndani ya muda mfupi na kuwavutia watu wengi”, alifafanua Shashu.

Aliongeza kuwa, “Tunamuomba sana Rais wetu atusaidie kutuletea umeme tuweze kuzalisha mawe ya kutosha ili serikali yenyewe ipate mapato makubwa na sisi wachimbaji na watu wengine wanaotegemea mgodi wetu tunufaike”, alisisitiza katibu huyo.





Na Paul Kayanda, Kahama

DIWANI wa Kata ya Majengo, Manispaa ya Kahama mkoani Shinyanga, Zacharia Shida Soko, ameendelea kuonyesha dhamira yake ya kuboresha sekta ya elimu katika kata hiyo baada ya kukabidhi mashine ya photocopy yenye thamani ya shilingi milioni 3.5 pamoja na karatasi (LIMU) kwa ajili ya kurahisisha upatikanaji wa mitihani katika Shule ya Msingi Anderson Msumba.

Mbali na mashine hiyo, Diwani Soko ametoa kiasi cha shilingi 600,000 kwa ajili ya kuwalipa walimu watatu wanaojitolea kufundisha katika shule hiyo, hatua inayolenga kuongeza nguvu kazi ya walimu na kuhakikisha wanafunzi wanapata elimu katika mazingira bora.

Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Soko amesema dhamira yake ni kuhakikisha Kata ya Majengo inafanya vizuri katika Manispaa ya Kahama, hususan katika sekta ya elimu ambayo ndiyo msingi wa maendeleo ya jamii.

“Kazi ni kuhakikisha Majengo inafanya vizuri katika Manispaa ya Kahama,” amesema Diwani Soko, huku akisisitiza kuwa atandelea kushirikiana na wananchi pamoja na wadau mbalimbali kuhakikisha changamoto za elimu zinatatuliwa.

Amewataka wanafunzi kujifunza kwa bidii na kuzingatia nidhamu shuleni na nyumbani, akisema wazazi wao wanahangaika na kujitoa kwa ajili ya kuhakikisha watoto wanapata elimu na baadaye kutimiza ndoto zao.

Soko amesema mafanikio katika jambo lolote, iwe katika elimu au biashara, yanahitaji nidhamu, hivyo amewataka wanafunzi kuifanya nidhamu kuwa sehemu ya maisha yao ya kila siku.

Katika kuhamasisha nidhamu na maadili, Diwani Soko ametangaza kuwa wanafunzi kumi watakaofanya vizuri katika suala la nidhamu shuleni watapatiwa zawadi, akisema hatua hiyo inalenga kuendeleza utamaduni wa nidhamu na maadili mema shuleni na nyumbani.

Hata hivyo Afisa Mtendaji wa Mtaa wa Sokola, Henry Mika Mayunga, amemshukuru Diwani Soko kwa hatua hiyo, akisema amekuwa msaada mkubwa kwa watoto katika shule za Kata ya Majengo, ikiwemo Anderson Msumba, Majengo na Mama Samia Sekondari.

Mayunga amesema Diwani huyo amekuwa akichangia pia upatikanaji wa chakula katika shule za kata yake, huku akieleza kuwa makabidhiano ya mashine hiyo yameondoa usumbufu uliokuwa ukiwakabili wazazi wa kuchangishwa fedha na watoto kwa ajili ya kutengeneza nakala za mitihani.

Mwenyekiti wa Mtaa wa Sokola, Patrobas Privatus, amesema Diwani Soko amekuwa akihakikisha kiwango cha elimu kinaongezeka katika shule za kata hiyo, akiamini kuwa mashine hiyo itasaidia kuongeza ufaulu kwa wanafunzi.

Privatus amemuomba Diwani huyo pia kushirikiana na viongozi wa dini kuwaleta walimu wa dini mbalimbali shuleni ili wanafunzi wapate malezi ya kiroho na maadili, akisisitiza kuwa suala la maadili linapaswa kupewa uzito katika malezi ya watoto.

Aidha, ameomba serikali inapotenga na kujenga shule mpya izingatie pia uwepo wa vyumba maalumu kwa ajili ya mafundisho ya dini, akisema hatua hiyo inaweza kusaidia katika kujenga kizazi chenye maadili mema.

Katibu wa CCM Kata ya Majengo, Sebabistian Masonga, amemtaka Diwani Soko kutokata tamaa katika juhudi zake za kuwaletea wananchi maendeleo, akiahidi kuwa chama kitaendelea kumuunga mkono kutokana na uchapakazi wake. Amesema vifaa na fedha alizokabidhi shuleni vina thamani ya zaidi ya shilingi milioni nne.

Masonga amesema Kata ya Majengo imewahi kuongozwa na madiwani mbalimbali, lakini haijawahi kuona kasi ya maendeleo kama ilivyo sasa.

Ameongeza kuwa ombi la mashine hiyo liliwasilishwa mbele ya Mbunge wa Jimbo la Kahama, Benjamin Ngayiwa, lakini Diwani Soko ameonyesha uwezo wa kulitatua kwa kulifanyia kazi moja kwa moja.

Kwa upande wake, Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Anderson Msumba, Scholastica Leonard, amesema msaada huo utawafanya wanafunzi kufanya mitihani bila kuchangishwa fedha na wazazi.

Amesema awali wazazi walikuwa wakichangia fedha za mitihani na karatasi, hali iliyosababisha baadhi ya wanafunzi kurudishwa nyumbani kutafuta fedha na hatimaye kuchangia utoro.

Mwenyekiti wa Kamati ya Shule, Saidi Kishimba John, amesema “kilio” chao kimepata suluhu na sasa wanailenga Anderson Msumba kupata matokeo ya daraja A, huku akisisitiza umuhimu wa nidhamu.







 



Na Oscar Assenga,TANGA

TUZO ya Taifa ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu imeendelea ,kuonyesha mafanikio makubwa, ambapo tangu kuanzishwa kwake Watanzania 27 wamefanikiwa kushinda katika nyanja mbalimbali za uandishi bunifu.

Hayo yamesema leo na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Tanga kuelekea zoezi la ukusanyaji Miswada ya Tuzo ya Taifa ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu 

Amesema mafanikio hayo yanaonyesha namna tuzo hiyo inavyoibua na kutambua vipaji vya waandishi bunifu nchini, huku idadi ya washiriki ikiongezeka kila mwaka kutoka ndani na nje ya Tanzania.

Prof. Mkenda amebainisha kuwa Serikali imewekeza takribani Shilingi milioni 800 kwa ajili ya kuchapisha vitabu vilivyoshinda tuzo hizo na kuvisambaza katika shule za Tanzania Bara na Zanzibar, hatua inayolenga kuwafikia wasomaji wengi zaidi na kuhamasisha utamaduni wa kusoma.

Aidha, Waziri Mkenda amesema tuzo hizo zimeendelea kukua na kuvutia washiriki kutoka mataifa mbalimbali, jambo linaloonyesha kuongezeka kwa hadhi yake na umuhimu wa uandishi bunifu katika kukuza fasihi na lugha ya Kiswahili.

Ameongeza kuwa tuzo hizo zimekuwa jukwaa la kuwahamasisha vijana na waandishi kutumia vipaji vyao katika kutengeneza kazi zenye ubunifu na maudhui yanayoweza kuelimisha na kujenga jamii.

“Tuzo hii sasa imeingizwa rasmi katika orodha ya tuzo za uandishi bunifu duniani, ukiitafuta mtandaoni utaona tarehe 13 Aprili ni siku ya kutoa Tuzo ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu,” amesema Prof. Mkenda.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Tuzo ya Taifa ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu, Prof. Penina Mlama, amesema dirisha la kuwasilisha miswada ya kazi za ubunifu limefunguliwa rasmi leo, Agosti 19, 2026, na litafungwa Novemba 30, mwaka huu.

Ameeleza kuwa waandishi bunifu wanatakiwa kutumia kipindi cha takribani miezi mitatu kuwasilisha miswada yao, huku matangazo yenye vigezo na taratibu za kushiriki yakitolewa kupitia mitandao ya kijamii ya tuzo hiyo pamoja na mitandao ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na Taasisi ya Elimu Tanzania.

Prof. Mlama amesema mshiriki anatakiwa kuwa raia wa Tanzania, kazi iwe imeandikwa kwa Kiswahili na kila mwandishi anaruhusiwa kuwasilisha andiko moja tu katika nyanja atakayochagua. Aidha, mswada unaowasilishwa unatakiwa kuwa haujawahi kuchapishwa popote.

Amefafanua kuwa miswada iliyowahi kushika nafasi ya kwanza hadi ya 10 katika miaka iliyopita haitaruhusiwa kuwasilishwa tena, ingawa waandishi waliowahi kushika nafasi hizo wanaweza kushiriki kwa kuwasilisha miswada mipya. Pia, miswada iliyowahi kushinda tuzo nyingine haitazingatiwa katika ushindani wa mwaka huu.

Kwa upande wa vigezo mahususi, tamthilia ya jukwaani inapaswa kutumia vionjo vya sanaa za maonyesho za Tanzania, iwe na muda wa dakika 40–60, isiwe na maonyesho zaidi ya sita na wahusika wasiozidi sita. Ushairi unatakiwa kuwa na mashairi yasiyopungua 50 wala kuzidi 60, huku kila shairi likiwa na beti zisizozidi 15.

Kwa riwaya, urefu unatakiwa kuwa kati ya maneno 60,000 na 100,000, wakati hadithi za watoto zinatakiwa kuwa na kati ya maneno 250 na 500 kwa hadithi moja. Prof. Mlama amesisitiza kuwa kazi zinazowasilishwa zinapaswa kuwa na mawazo asilia ya mwandishi na kujikita katika masuala muhimu ya jamii.

Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar ambae pia ni wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amempongeza Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Ndg. Abdi Mahmoud Abdi, kwa uteuzi wake na kumtaka kutekeleza majukumu yake kwa bidii, huku akiahidi kumpatia ushirikiano zaidi.

Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 19 Agosti 2026, alipokutana na Ndg. Abdi Mahmoud Abdi, aliyefika Ikulu Zanzibar kujitambulisha rasmi kufuatia uteuzi wake kuwa Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, pamoja na kupokea maelekezo kuhusu utekelezaji wa majukumu yake mapya.

Amesema ana imani na uwezo wake kutokana na uzoefu na utendaji aliouonesha alipokuwa Naibu Katibu Mkuu wa UVCCM Zanzibar, huku akisisitiza umuhimu wa kushirikiana na viongozi na watendaji wa Chama katika kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu CCM Zanzibar Ndg. Abdi Mahmoud Abdi amemshukuru Rais Dkt. Mwinyi kwa ushauri na maelekezo aliyompatia, na kuahidi kufanya kazi kwa bidii na kushirikiana na viongozi na watendaji wenzake katika kutekeleza majukumu ya Chama.








Na Mwandishi Wetu, Shinyanga

SERIKALI imesema itaendelea kuongeza nguvu katika mapambano dhidi ya maambukizi ya Virusi vya UKIMWI (VVU), kwa kuboresha vituo vya huduma, kuwezesha vikundi na kuimarisha ushirikiano na wadau, ili kuhakikisha Tanzania inafikia lengo la kutokomeza UKIMWI ifikapo mwaka 2030.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dk. Jim Yonazi, wakati wa ziara yake mkoani Shinyanga, ambapo alitembelea vikundi mbalimbali vya vijana vinaoishi na Maambukizi ya VVU pamoja na Kituo cha Maarifa Kahama kilichopo Kagongwa mkoani humo.

Dk. Yonazi amesema juhudi zinazofanywa na Serikali kwa kushirikiana na wadau zimeanza kuzaa matunda, huku akisisitiza umuhimu wa kuongeza kasi katika utoaji wa elimu, upimaji, ushauri nasaha, pamoja na huduma za tiba na matunzo kwa watu wanaoishi na VVU.

“Lengo ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma karibu nao, lakini vilevile wanapata elimu inayowasaidia katika mapambano dhidi ya UKIMW na maambukizi ya UKIMWIi,” amesema.

Amesema Serikali imeendelea kuboresha huduma hizo ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma kwa wakati, huku akiwataka wadau kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuimarisha afua za kukabiliana na VVU.

Dkt. Yonazi amepongeza Mkoa wa Shinyanga kwa kufikia malengo ya kimataifa ya 95-95-95, akisema hatua hiyo ni ishara ya mafanikio katika jitihada za kupunguza maambukizi mapya na madhara yatokanayo na VVU.

“Serikali imeamua kwa makusudi kabisa kuongeza nguvu yake. Ndiyo maana imeanzisha Mfuko wa Mfadhili, na asilimia 70 ya fedha hiyo inakwenda katika Mfuko wa UKIMWI ili kusaidia afua mbalimbali na kuondokana na utegemezi,” amesema.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga,Mhe. Mbona Mahita, alisema mkoa huo bado una kiwango cha maambukizi ya VVU kilicho juu ya wastani wa kitaifa, ambapo Shinyanga ina asilimia 5.6 ikilinganishwa na asilimia 4.4 ya kitaifa.

Mahita alisema Serikali imeendelea kuongeza elimu kuhusu VVU katika ngazi mbalimbali, kuanzia kaya hadi jamii, ili wananchi wawe na uelewa wa kutosha kuhusu namna ya kujikinga na maambukizi.

“Shinyanga ni business hub kwa Kanda ya Ziwa. Movement za watu mara kwa mara ni kubwa. Watu wanaoingia na kutoka ni wengi, ndiyo maana tumeshuka mpaka kwenye ngazi za kijamii katika utoaji wa elimu,” alisema.

Awali, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Dk. Honoratha Rutatinisibwa, alisema mkoa huo una vituo 374 vinavyotoa huduma za afya, ambapo vituo 120, sawa na asilimia 32, vinatoa huduma za tiba na matunzo kwa watu wanaoishi na VVU.

Dkt. Rutatinisibwa amesema, kwa mujibu wa utafiti wa maambukizi ya VVU uliofanyika mwaka 2023, kiwango cha maambukizi mkoani Shinyanga ni asilimia 5.6, ikilinganishwa na wastani wa kitaifa wa asilimia 4.4.

Akizungumzia huduma zinazotolewa katika Kituo cha Maarifa Kahama kilichopo Kagongwa, Mratibu wa Kudhibiti Maambukizi ya VVU, Homa ya Ini na Magonjwa ya Ngono Kahama, Dkt. Herry Silvester, amesema kituo hicho kinatoa huduma za tiba na matunzo, pamoja na huduma maalumu kwa makundi yaliyo katika mazingira hatarishi.

Amesema makundi hayo ni pamoja na madereva wa masafa marefu, mabinti na wanawake vijana, ambao wamekuwa wakifikiwa kupitia huduma za upimaji, elimu na ushauri nasaha. 



Na Said Mwishehe,Michuzi TV 

WIZARA ya Maliasili na Utalii imetangaza rasmi kufunguliwa kwa dirisha la usajili kwa wadau wa uhifadhi na utalii kuwania The Serengeti Awards 2026, huku ikiwasisitiza kutumia fursa hiyo kuonyesha kazi, ubunifu na mafanikio yao katika uhifadhi na uendelezaji wa utalii.

Akizungumza leo Agosti 19,2026 jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Idara ya Utalii, Dk. Thereza Mugobi, amesema dirisha la usajili litafunguliwa Agosti 20, 2026 na kufungwa Septemba 30, 2026, kupitia tovuti rasmi ya tuzo hizo www.serengetiawards.go.tz, ambako wadau watapata taarifa kuhusu kategoria, vigezo na taratibu za kushiriki.

Amefafanua Serengeti Awards zinafanyika kwa mara ya pili ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali za kutambua, kuthamini na kuenzi mchango wa wadau katika uhifadhi wa maliasili na urithi wa Taifa pamoja na uendelezaji wa utalii.

“Tuzo hizi zinalenga pia kutoa motisha kwa wadau kuboresha utendaji, kuhamasisha ubunifu na kuongeza ushindani wa Destination Tanzania,” amesema Dk. Mugobi na kuongeza mwaka huu kutakuwa na kategoria 63 katika makundi saba, ambayo ni People’s Choice Awards, Tourism Operator Awards, Tourism Guide Awards, Best Accommodation and Restaurant Services, Conservation Awards, Tourism Exhibitor Awards na Special Appreciation Awards.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Ufundi ya Serengeti Awards, Hatibu Madudu, amesema idadi ya kategoria imeongezeka kutoka 56 mwaka jana hadi 63 mwaka huu, baada ya kupokea maoni kutoka kwa wadau na kufanya maboresho katika mchakato wa tuzo.

Madudu amesema baadhi ya maboresho yamezingatia changamoto zilizobainika katika mchakato wa mwaka uliopita, huku wananchi wakitarajiwa kushiriki katika mchakato wa kuwapata washindi wa baadhi ya kategoria.

Wadau kutoka ndani na nje ya Tanzania wanaruhusiwa kuwania tuzo hizo iwapo watatimiza vigezo vilivyowekwa. Serikali imewahakikishia wadau kuwa mchakato wa Serengeti Awards 2026 utasimamiwa kwa kuzingatia uwazi, usawa na uadilifu.







Na Mwandishi Wetu


CHUO cha Future World Vocational Institute kilichopo Chanika, Dar es Salaam, kimewahimiza wazazi kuwapeleka vijana kupata mafunzo ya ufundi yatakayowawezesha kupata ajira au kujiajiri.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Agosti 18,2026, Meneja Masoko wa chuo hicho, David Msumba, amesema mafunzo hayo yanalenga kuwapatia vijana ujuzi wa vitendo unaowawezesha kushindana katika soko la ajira na pia kuanzisha shughuli zao wenyewe.

Amesema chuo hicho kimeamua kuimarisha mafunzo ya ufundi kutokana na changamoto ya ajira inayowakabili vijana wengi wanaomaliza masomo bila kuwa na ujuzi wa moja kwa moja unaoweza kuwawezesha kujiajiri.

Msumba amesema mabadiliko katika mfumo wa elimu nchini, yanayosisitiza umuhimu wa kuunganisha elimu na ujuzi wa vitendo, yanaongeza haja kwa vijana kupata mafunzo ya ufundi ili kuwa na uwezo wa kujitegemea kiuchumi.

“Kozi hizi zinatoa fursa ya moja kwa moja ya ajira kwa vijana wetu, lakini pia zinawapa nafasi ya kujiajiri na kuanzisha shughuli zao wenyewe,” amesema Msumba.

Ameongeza chuo hicho pia kimeweka utaratibu wa malipo ya ada kwa awamu ili kuwawezesha wazazi wenye uwezo tofauti wa kifedha kuwapeleka watoto wao kupata mafunzo hayo bila mzigo wa kulipa ada yote kwa mara moja.

Kwa mfano, amesema kozi ya umeme wa majumbani inagharimu Sh950,000 kwa mwaka, ambapo mzazi anaweza kulipa kwa awamu nne.

Mbali na mafunzo, Msumba amesema chuo hicho kinatoa huduma ya hostel kwa wanafunzi wanaotoka maeneo ya mbali, hatua inayolenga kuwawezesha vijana wengi zaidi kunufaika na fursa hiyo.

Ametoa mwito kwa wazazi na vijana wa Chanika na maeneo mengine ya Dar es Salaam kutumia fursa hiyo kupata ujuzi wa ufundi utakaowawezesha kupata ajira, kujiajiri na kujenga msingi wa maisha ya kujitegemea.






Top News