Na Mwandishi Wetu Zanzibar
YAS Fiber Tanzania itawekeza takriban shilingi bilioni 300 kwa kipindi cha miaka 20 ili kupanua huduma za intaneti yenye kasi visiwani Zanzibar kufuatia kusainiwa kwa makubaliano ya Ushirikiano kati ya kati ya Shirika la Mawasiliano Zanzibar (ZICTIA), Wizara ya Kazi na Uwekezaji Zanzibar na Yas Fiber.

Uwekezaji huo unatarajiwa kuwezesha huduma za mkonga wa mawasiliano (fiber) katika kuzifikia takriban kaya 100,000 katika visiwa vya Unguja na Pemba ndani ya miaka mitatu ya kwanza ya utekelezaji wa mradi.

Makubaliano hayo yanaashiria hatua muhimu katika juhudi za kuimarisha miundombinu ya kidigitali Zanzibar na kuongeza upatikanaji wa huduma za intaneti za uhakika, nafuu na zenye kasi kwa kaya, biashara, taasisi za elimu, vituo vya afya na taasisi za Serikali. Aidha, yanaunga mkono azma ya Zanzibar ya kujiimarisha kama kitovu cha ubunifu, uwekezaji na huduma za kidigitali.

Akizungumza wakati wa hafla ya utiaji saini wa makubaliano hayo, Waziri wa Mawasiliano, Teknolojia ya Habari na Ubunifu Zanzibar, Mhe. Mudrick Ramadhan Soraga, alisema ushirikiano huo unaonesha dhamira ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kutumia teknolojia kama nyenzo ya kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

"Miundombinu ya kidigitali ni msingi wa uchumi wa kisasa. Ushirikiano huu utaharakisha mageuzi ya kidigitali na kusaidia kuiweka Zanzibar katika nafasi ya kuwa miongoni mwa vinara wa uchumi wa kidigitali katika ukanda wa Afrika Mashariki," alisema Mhe. Soraga.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa ZICTIA, Mhandisi Shukuru Awadh Suleiman, alisema makubaliano hayo yataongeza kasi ya upanuzi wa huduma ya mkonga wa mawasiliano visiwani humo na kusaidia kuimarisha upatikanaji wa huduma bora za mawasiliano kwa wananchi

"Ushirikiano huu utawezesha wananchi na taasisi nyingi zaidi kupata huduma za intaneti yenye kasi na kuchangia ujenzi wa miundombinu ya kidigitali inayohitajika kwa maendeleo ya Zanzibar ya sasa na ya baadae," alisema Mhandisi Suleiman.

Naye Afisa Mtendaji Mkuu wa Yas Fiber, Maxime Woimant, alisema uwekezaji huo unaonesha dhamira ya kampuni hiyo katika kuunga mkono ajenda ya mageuzi ya kidigitali nchini na maendeleo jumuishi kupitia mawasiliano ya kisasa."Huu ni miongoni mwa uwekezaji mkubwa zaidi wa miundombinu ya kidigitali kuwahi kufanyika Zanzibar katika miaka ya hivi karibuni.

Kupitia ushirikiano huu, tutapanua upatikanaji wa huduma za intaneti za viwango vya kimataifa zitakazowezesha biashara kukua, wanafunzi kujifunza, ubunifu kwa taasisi na jamii kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kidigitali," alisema Woimant.

Aliongeza kuwa Yas Fiber inajiona si mwekezaji pekee bali mshirika wa maendeleo wa muda mrefu anayelenga kupanua fursa za kijamii na kiuchumi kupitia mawasiliano ya uhakika na ya kisasa.Mradi huo utatekelezwa chini ya mfumo wa Ushirikiano kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP), ukiunganisha maono ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kujenga uchumi wa kidigitali na uzoefu wa Yas Fiber katika kubuni, kuwekeza, kujenga, kuendesha na kusimamia huduma ya Fiber-to-the-Home (FTTH).Upatikanaji bora wa huduma za intaneti unatarajiwa kuchochea ubunifu, ujasiriamali, elimu ya kidigitali, huduma za serikali mtandao (e-Government) na utoaji wa huduma za afya za kisasa, huku ukiimarisha zaidi mvuto wa Zanzibar kama kitovu cha uwekezaji, utalii na biashara katika ukanda huu.

Serikali ya Zanzibar kupitia Shirika la Mawasiliano Zanzibar (ZICTIA) itatoa ushirikiano katika masuala ya upatikanaji wa maeneo ya utekelezaji, uratibu wa kikanuni na usimamizi wa mradi ili kuhakikisha utekelezaji wake unafanikiwa.Mbali na uwekezaji wa miundombinu, ushirikiano huo pia utachangia maendeleo ya ujuzi wa kidigitali, uhamishaji wa maarifa na kujenga uwezo wa wataalamu wa ndani, hatua itakayosaidia kuandaa kizazi kijacho kushindana katika uchumi unaoendeshwa na teknolojia na kuunga mkono maono ya muda mrefu ya Zanzibar ya kuwa kitovu kinachoongoza kwa uchumi wa kidigitali Afrika Mashariki.

Akizungumza wakati wa hafla ya utiaji saini huo, Waziri wa Mawasiliano, Teknolojia ya Habari na Ubunifu Zanzibar, Mudrik Ramadhan Soraga, alisema ushirikiano huo ni sehemu ya jitihada za Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanapata huduma bora za mawasiliano na kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kidijitali.

Alisema tayari utekelezaji wa mradi huo umeanza kabla hata ya kutiwa saini kwa makubaliano hayo, jambo linalodhihirisha dhamira ya dhati ya pande zote mbili katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma hizo kwa haraka.











Na Mwandishi Wetu

WAFUGAJI nchini wamefurahishwa na mpango wa matumizi ya Mfumo wa Stakabadhi za Ghala kwenye sekta ya mifugo wakidai kuwa utaleta manufaa makubwa katika masoko na biashara shindani ya mifugo.

Akizungumza baada ya kutembelea banda la Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) katika Maonesho ya Mifugo na Mnada wa Kimataifa yanayofanyika katika Shamba la Mbogo, Chalinze mkoani Pwani, Mwenyekiti wa Chama Cha Wafugaji Tanzania (CCWT), Mrida Mshota, amesema mfumo huo utasaidia kutatua changamoto ya masoko ya mifugo nchini.

Amesema kupitia mpango huo wafugaji watapata fursa ya kujitangaza katika masoko ya kimataifa na kuuza mifugo yao kwa uhakika zaidi.

“Ukiwa na shamba lako na likasajiliwa na serikali sasa unakuwa na uhakika wa kuuza mifugo kwenye masoko makubwa ya kimataifa. Mpango huu ni mzuri na naiomba serikali iweke mkazo mkubwa kuhakikisha unaanza kutekelezwa haraka. Waziri Mkuu tayari alishasema jambo hili lishughulikiwe kwa haraka ili liwe na tija kwa wafugaji,” amesema Mshota.

Aidha, ameishauri Wizara ya Viwanda na Biashara kuweka mikakati madhubuti katika maeneo mbalimbali nchini ili utekelezaji wa mfumo huo uanze kabla ya mwaka huu kuisha.

“Sisi tuna kanda nane, hivyo tukitumia vizuri kanda zote serikali itakwenda kukusanya mapato bila kutumia nguvu kubwa. Kwa sasa utoroshaji wa mifugo ni mkubwa kwani baadhi ya wafugaji wanapeleka mifugo nje ya nchi bila utaratibu rasmi, lakini tukianza kutumia mfumo huu wenye masoko ya uhakika, tatizo hilo litapungua kwa kiasi kikubwa,” amesema.

Naye, Afisa Ubora wa WRRB, Bw. Anatolius Kabyemera, amesema mfumo huo utaleta uwazi katika biashara ya mazao na mifugo, kuongeza ushindani wa bei na kuhakikisha wafugaji pamoja na wakulima wanapata thamani halisi ya bidhaa zao.
Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima (TEWW) imeeleza kuwa ina mchango mkubwa katika kuwawezesha watoto, vijana na watu wazima waliokosa fursa ya elimu ndani ya mfumo rasmi kurejea na kuendelea na masomo yao.

Hayo yameelezwa na Mkuu wa Taasisi hiyo, Profesa Philipo Sanga, wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dodoma Juni 22, 2026, kwenye maadhimisho ya Wiki ya utumishi wa Umma.

Ameeleza majukumu makubwa ya TEWW ni kushughulikia elimu ya watu wazima na elimu nje ya mfumo rasmi, sekta ambayo imekuwa muhimu katika kuwasaidia wananchi wengi kupata elimu na ujuzi unaohitajika katika maisha na maendeleo ya taifa.

Amesema takwimu zinaonyesha kuwa kati ya kila watoto 10 kwa baadhi ya maeneo, watoto wanne hawapati fursa ya kuanza shule, huku kundi kubwa la wanafunzi likikatisha masomo katika ngazi mbalimbali za elimu.

“Katika kila wanafunzi 100, takribani 31 hudondoka na kushindwa kuendelea na masomo kwa ujumla, zaidi ya wanafunzi laki nne kutoka shule za msingi na sekondari hudondoka kila mwaka na kukosa fursa ya kuendelea na elimu."

Amebainisha kuwa bila uwepo wa Taasis ya Elimu ya Watu Wazima, idadi kubwa ya wananchi wengi wangeshindwa kupata nafasi ya kurejea katika mfumo wa elimu na kufikia malengo yao.

Kwa mujibu wa Profesa Sanga, Taasisi hiyo inatekeleza miradi mbalimbali ya elimu ya msingi na sekondari nje ya mfumo rasmi, inayolenga kuwapa wananchi fursa ya kupata elimu, maarifa na ujuzi unaowawezesha kujitegemea na kuchangia maendeleo ya taifa.

Aidha, amesema TEWW kupitia Chuo cha Elimu ya Juu cha Elimu ya Watu Wazima hutoa programu za elimu kuanzia ngazi ya cheti, stashahada, shahada hadi shahada za uzamivu kwa lengo la kuandaa wataalamu wabobevu watakaosaidia maendeleo ya nchi.

Ameongeza kuwa katika kila mkoa kuna viongozi wa elimu ya watu wazima wanaosimamia shughuli za taasisi hiyo na kuhakikisha huduma zinawafikia wananchi katika maeneo mbalimbali.

Aidha ameeleza changamoto mbalimbali zinazowakabili wanafunzi ndiyo chanzo kikuu cha kudondoka kwao kielimu, hivyo taasisi hiyo imejikita katika kuwasaidia kurejea masomoni na kutimiza ndoto zao za elimu.

Kwa upande wa elimu ya juu, Profesa Sanga amesema Taasis ya Elimu ya Watu Wazima imefanikiwa kudahili zaidi ya wanafunzi 6,000 na kwamba zaidi ya wanafunzi 2,000 huhitimu kila mwaka, jambo linaloonyesha mchango mkubwa wa taasisi hiyo katika kuboresha sekta ya elimu nchini.

Profesa Sanga amesema kupitia banda la TEWW katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea Jijini Dodoma hadi Juni 23, wananchi wanaweza kupata huduma mbalimbali ikiwemo taarifa za udahili na matumizi ya mfumo wa kutunza takwimu za elimu nje ya mfumo rasmi.


Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

NAIBU Waziri wa Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Regina Ndege Qwaray, amesema lengo la Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) ni kuwawezesha wananchi wanaoishi katika mazingira magumu na kaya maskini kujikwamua kiuchumi, kufikia ndoto zao na kuboresha maisha yao kwa kujitegemea.

Regina ametoa kauli hiyo leo alipokuwa akitembelea banda la TASAF katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma.

Amesema TASAF imeendelea kufanya kazi kubwa ya kuelimisha wananchi kuhusu fursa mbalimbali zinazotolewa na mfuko huo, hatua ambayo imeongeza uelewa kwa kaya maskini na kuwasaidia kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo.

"Nawapongeza TASAF kwa kazi nzuri mnayoifanya. Msichoke kuendelea kumsaidia Mheshimiwa Rais katika kutekeleza majukumu ya kuwainua wananchi kiuchumi na kuifanya Tanzania kuwa imara kwa kuwawezesha watu kujitegemea badala ya kutegemea misaada," amesema Regina.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Singida, Halima Dendego, ameipongeza TASAF kwa kuendelea kutoa msaada wa elimu kwa watoto kutoka katika kaya maskini, jambo ambalo limechangia kuwawezesha kuendelea na masomo yao huku familia zao zikipata nafuu ya changamoto za kiuchumi.

Amesema uwekezaji katika elimu kupitia TASAF umekuwa na mchango mkubwa katika kujenga mustakabali bora wa watoto wanaotoka katika mazingira yenye uhitaji mkubwa.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Pangani, Gift Msuya, amesema viongozi wa wilaya hukutana na watoto wengi wenye uwezo mkubwa wa kitaaluma lakini wanakabiliwa na changamoto za kifedha zinazowazuia kufikia malengo yao ya elimu.

Kutokana na hali hiyo, ameshauri TASAF kuangalia uwezekano wa kuwa na mfumo utakaotambua kaya zenye uhitaji kupitia mamlaka za serikali za mitaa, ikiwemo zile zilizopo maeneo ya mijini ambazo mara nyingi hushindwa kuingia kwenye mifumo ya TASAF kupitia utaratibu wa kawaida wa usajili.

"Tuna kaya nyingi zenye uhitaji mkubwa mijini ambazo hazijafikiwa na programu za TASAF. Ni muhimu kuangalia namna ya kuzitambua na kuzifikia ili nazo zipate fursa ya kunufaika na huduma hizi," amesema Msuya.

Aidha, ameomba TASAF kuzingatia zaidi kaya zenye watoto yatima waliofiwa na wazazi wao, ili waweze kupata msaada unaohitajika na kuendelea na masomo pamoja na maisha yao ya kila siku bila vikwazo vikubwa vya kiuchumi.

Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yameendelea kuwa jukwaa muhimu kwa taasisi mbalimbali za serikali kuonyesha huduma wanazotoa kwa wananchi pamoja na mafanikio yaliyopatikana katika kuboresha ustawi wa jamii.




 


Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma

Mbunge wa Kigoma Mjini Clayton Revocatus Chipando (Baba levo) ameishauri Serikali na Bunge kufanya mapitio ya mfumo wa utozaji tozo katika sekta ya bodaboda, akisisitiza kuwa kundi hilo kubwa la vijana haliwezi kubebeshwa mzigo mpya wa kodi kutokana na hali yao ya kiuchumi.

Akichangia mjadala wa bajeti kuu ya Serikali, Chipando amesema bodaboda ni moja ya sekta zinazowezesha maisha ya mamilioni ya Watanzania, na kuongeza gharama mpya kutawaumiza zaidi wananchi walioko katika kipato cha chini.

Ameeleza kuwa takribani asilimia 75 ya waendesha bodaboda nchini ni vijana waliomaliza elimu ya msingi, hususan darasa la saba, ambao hawakuweza kuingia katika ajira rasmi, hivyo kujikuta wakijiajiri kwenye sekta isiyo rasmi ili kujikimu kimaisha.

Amesema badala ya kuongeza tozo katika sekta hiyo, Serikali inapaswa kutafuta vyanzo vingine vya mapato visivyoathiri moja kwa moja wananchi wenye kipato kidogo, huku akilinganisha hali hiyo na ongezeko la gharama katika bidhaa nyingine ambazo hazina athari kubwa kwa kundi hilo.

Katika hoja nyingine, mbunge huyo ameitaka Serikali kuwekeza zaidi kwenye teknolojia ya kisasa katika sekta ya ulinzi, ikiwemo matumizi ya ndege zisizo na rubani (drone) na vifaa vya kisasa vya kijeshi, ili kuendana na mabadiliko ya vita vya kisasa duniani, akitolea mfano wa migogoro kama ya Ukraine.

Aidha, katika sekta ya michezo na sanaa, Chipando amependekeza taasisi za kifedha kuwapa wasanii muda wa kutosha wa kurejesha mikopo wanayopewa kupitia programu za Serikali. Ameomba muda wa angalau miezi mitatu hadi sita ili kuwapa nafasi ya kurejesha mikopo baada ya kazi zao kuanza kuleta kipato.

Pia amesisitiza kuwa mikopo hiyo, ambayo hutolewa kupitia Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Samia Suluhu Hassan, inapaswa kuwa na masharti rafiki yanayolenga kuwawezesha walengwa kunufaika badala ya kubanwa na ratiba ngumu za marejesho.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza jambo na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt, Netumbo Nandi-Ndaitwah baada ya Rais huyo wa Namibia kuhitimisha Ziara yake ya Kitaifa ya siku 4 katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 22 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa amesimama na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah wakati wakipokea heshima ya Wimbo wa Taifa katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam kabla ya Rais huyo wa Namibia kuhitimisha Ziara yake ya Kitaifa ya siku 4 nchini Tanzania, tarehe 22 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza jambo na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt, Netumbo Nandi-Ndaitwah baada ya Rais huyo wa Namibia kuhitimisha Ziara yake ya Kitaifa ya siku 4 katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 22 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiagana na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt, Netumbo Nandi-Ndaitwah katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 22 Juni, 2026. Rais Mhe. Dkt. Ndaitwah amehitimisha Ziara yake ya Kitaifa ya siku 4 nchini Tanzania ambapo pamoja na kufanya mazungumzo na Rais Mhe. Dkt. Samia pia alitembelea Kambi ya Kihistoria ya Wapigania Uhuru wa nchi yake, Kongwa mkoani Dodoma.


atukio mbalimbali wakati Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt, Netumbo Nandi-Ndaitwah akihitimisha Ziara yake ya Kitaifa ya siku 4 nchini Tanzania, katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 22 Juni, 2026.

📍DODOMA

Banda la Tume ya Madini limeendelea kuwa kivutio kikubwa kwa mamia ya wananchi wanaotembelea Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma, huku wengi wakijitokeza kupata elimu kuhusu sekta ya madini, huduma zinazotolewa na Tume  pamoja na fursa zilizopo katika shughuli za utafutaji, uchimbaji na biashara ya madini.

Miongoni mwa waliotembelea banda hilo ni Lusajo Luena kutoka Dodoma, ambaye amesema elimu aliyoipata imemwezesha kuelewa taratibu za upatikanaji wa leseni za madini na wajibu wa wamiliki wa leseni katika kuendeleza maeneo yao ya uchimbaji.

"Kabla ya kufika hapa sikuwa na uelewa wa kina kuhusu namna leseni za madini zinavyotolewa na kusimamiwa. Leo nimepata elimu ya kutosha kuhusu taratibu mbalimbali na umuhimu wa kuzingatia sheria za madini," amesema Luena.

Kwa upande wake, Joyce Kitundu kutoka Dodoma amesema maelezo aliyopata katika banda hilo yamemsaidia kufahamu mchango mkubwa wa sekta ya madini katika ukuaji wa uchumi wa taifa na namna Serikali inavyosimamia rasilimali za madini kwa manufaa ya wananchi.

"Nimejifunza kuwa sekta ya madini ni nguzo muhimu ya maendeleo ya nchi. Pia nimeelewa majukumu ya Tume ya Madini katika kusimamia shughuli za uchimbaji na biashara ya madini nchini," amesema Kitundu.

Naye Glory Daudi kutoka Kondoa amesema elimu aliyopata imefungua fursa mpya za uelewa kuhusu ushiriki wa vijana na wanawake katika shughuli mbalimbali zinazohusiana na sekta ya madini.

"Nimefurahishwa na elimu niliyopewa kuhusu fursa zilizopo kwenye sekta ya madini. Sasa nimeelewa kuwa si lazima mtu awe mchimbaji pekee, kwani kuna fursa nyingi za biashara na utoaji huduma zinazozunguka sekta hii," amesema Daudi.

Tume ya Madini inaendelea kutumia maonesho hayo kutoa elimu kwa umma kuhusu majukumu yake, huduma mbalimbali zinazotolewa pamoja na kuhamasisha ushiriki wa Watanzania katika mnyororo mzima wa thamani wa sekta ya madini ili kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini.








Asubuhi ya Jumamosi, tarehe 11 Julai 2026, mitaa ya Dar es Salaam itasimama kama kumbukumbu hai na alama ya heshima kwa urithi wa usanifu, kwani kutakuwa na Matembezi ya Kumbukumbu ya Miaka Kumi ya Mbunifu Majengo Beda Amuli — yenye kaulimbiu ndogo ya “Kutembea Ndani ya Urithi” — yatawakutanisha wasanifu majengo, wapangaji miji, wanafunzi, wanahistoria na wananchi kwa ujumla katika matembezi ya kuongozwa ya alfajiri, yakipita kwenye maeneo muhimu yenye alama ya mchango wa mmoja wa watu mashuhuri zaidi katika historia ya usanifu wa majengo nchini Tanzania.

Tukio hilo, lililoandaliwa na familia ya marehemu mbunifu huyo kwa kushirikiana na Chama cha Wasanifu Majengo Tanzania, Architectural Association of Tanzania (AAT), chini ya kaulimbiu “Kubuni Tanzania: Usanifu kwa Watu, Mahali na Madhumuni”, litaanzia katika Jengo la Old Boma, moja ya majengo ya kihistoria zaidi ya Dar es Salaam kutoka enzi za ukoloni. Usajili na ugawaji wa T-shirt utaanza saa 12:00 asubuhi, ufunguzi rasmi utafanyika saa 12:30 asubuhi, na matembezi yataanza saa 1:00 asubuhi kamili.

Njia ya Matembezi: Jiji Linajisoma kwa Sauti
Yakiondoka katika Jengo la Old Boma saa 1:00 asubuhi, matembezi hayo yatapitia mlolongo maalumu wa maeneo yaliyochaguliwa kwa umakini. Kituo cha kwanza kitakuwa eneo la Kilimanjaro / Hyatt saa 1:10 asubuhi, kikifuatiwa na Kituo cha Pili katika Jengo la IFM saa 1:25 asubuhi, na Kituo cha Tatu katika Jengo la Ushirika la Taifa saa 1:40 asubuhi.

Matembezi hayo yatahitimishwa katika Soko la Kariakoo, kitovu cha biashara cha jiji, saa 2:05 asubuhi, yakifuatiwa na maoni ya washiriki, mazungumzo na vyombo vya habari, pamoja na ufungaji rasmi saa 2:30 asubuhi.

Na Janeth Raphael - MichuziTv -Dodoma 

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imepokea msaada wa Euro milioni 20, sawa na Shilingi bilioni 60.7, kutoka Serikali ya Shirikisho la Jamhuri ya Ujerumani kupitia Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KfW) kwa ajili ya kutekeleza Mradi wa Uboreshaji wa Huduma za Usambazaji Maji na Usafi wa Mazingira katika miji ya Tunduma na Vwawa-Mlowo mkoani Songwe. Msaada huo ulirasimishwa kupitia utiaji saini wa mkataba kati ya pande hizo mbili.

Akizungumza katika hafla ya utiaji saini wa mkataba huo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu  Mwamba, alisema mradi huo unalenga kuboresha upatikanaji endelevu wa maji safi na salama pamoja na huduma za usafi wa mazingira kwa wakazi wa maeneo husika. 

Alieleza kuwa utekelezaji wa mradi huo utahusisha ujenzi wa miundombinu ya usambazaji maji, kuunganisha wateja wapya, kujenga mtambo wa kutibu majitaka, kununua magari ya kuvuta majitaka na kujenga miundombinu ya usafi katika taasisi za umma ikiwemo vyoo vya shule zilizochaguliwa.

Dkt. Mwamba ameishukuru Serikali ya Ujerumani kwa kuendelea kuwa mshirika muhimu wa maendeleo wa Tanzania kupitia ufadhili wa miradi mbalimbali inayotekelezwa katika sekta za maji, afya, uhifadhi wa maliasili na mazingira, usimamizi wa fedha za umma pamoja na usawa wa kijinsia. Alisema misaada hiyo imekuwa na mchango mkubwa katika kukuza maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.

Aidha, amekumbusha kuwa wakati wa majadiliano ya ushirikiano wa maendeleo kati ya Tanzania na Ujerumani yaliyofanyika Machi 20, 2024 jijini Dar es Salaam, Serikali ya Ujerumani iliahidi kutoa Euro milioni 70 kwa ajili ya kufadhili miradi mbalimbali nchini. 

Alieleza kuwa msaada uliosainiwa sasa ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi hiyo na unaonesha kuendelea kuimarika kwa uhusiano wa muda mrefu kati ya mataifa hayo mawili.

Dkt. Mwamba amesisitiza dhamira ya Serikali ya Tanzania chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuendeleza ushirikiano wa maendeleo na Ujerumani, huku akiahidi kuwa serikali itachukua hatua zote muhimu kuhakikisha miradi yote inayofadhiliwa inatekelezwa kwa ufanisi ili kufikia malengo yaliyokusudiwa na kuwanufaisha wananchi.

Naye Mkurugenzi Mkazi benki ya Maendeleo Ujerumani Vanessa Eidt amesema ushirikiano Baina ya Tanzania na Ujerumani utaendelea kuleta matunda kwa wananchi wa Tanzania na anaamini mradi huo utakqenda kutekelezwa kama ulivyopamgwa na kunufaisha wananchi wa maeneo hayo Kupata majie safi na ya uhakika.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Maji. mhandisi Mwajuma  Waziri amesema mradi huo umefika wajati muafaka kwani kuna mabadiliko ya tabia nchi pamoja na ukuaji wa kasi wa miji inayoongwza shinikizo katika rasilimali za maji, hivyo utekelezaji wa mradi huo utaimarisha usimamizi wa rasilimali za maji unaozingatia mabadikiko ya tabia nchi na kuboresha upatikanaji wa maji kwa uhakika katika maeneo hayo.

Hata hivyo Mhandisi Mwajuma amesema wizara ya maji itaendelea kuhakikisha mradi huo unatekelezaa kwa ufanisi, uwazie na kwa wakati kwa kushirikisha kwa karibu na wadau ili kuhakikisha unaleta manufaa ya kudumu kwa wananchi wa Tanzania.






Vijana katika mikoa tisa nchini wanatarajiwa kunufaika na Programu ya Mifumo Himilivu ya Chakula inayotekelezwa na Wizara ya Kilimo kwa lengo la kuongeza ushiriki wao katika sekta ya kilimo kupitia matumizi ya teknolojia za kisasa na miradi ya umwagiliaji inayotarajiwa kuanza mwaka ujao.

Akizungumza na waandishi wa habari Juni 22, 2026, wakati wa Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma jijini Dodoma, Mtaalamu wa Masuala ya Vijana, Laurean Masele, amesema programu hiyo inalenga kuwajengea vijana uwezo wa kujiajiri na kuongeza kipato kupitia kilimo chenye tija.

Amesema mikoa inayonufaika na programu hiyo ni Tanga, Arusha, Kilimanjaro, Dodoma, Pwani, Morogoro, Njombe, Iringa na Mbeya, ambapo vijana wanahamasishwa kujiunga na shughuli za kilimo cha kisasa kupitia halmashauri za maeneo husika.

Masele amesema programu hiyo imeweka mkazo kwenye kilimo cha mazao ya bustani kama nyanya na vitunguu ambavyo hukomaa kwa muda mfupi na kuwawezesha vijana kupata kipato kwa haraka.

Aidha, utekelezaji wa skimu za umwagiliaji pamoja na uchimbaji wa visima kwa wakulima wadogo unatarajiwa kuongeza upatikanaji wa maji kwa shughuli za kilimo na kuifanya sekta hiyo kuwa ya kuvutia zaidi kwa vijana.

Ameeleza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya juhudi za serikali za kubadilisha mtazamo wa vijana kuhusu kilimo na kukifanya kuwa chanzo muhimu cha ajira na maendeleo ya kiuchumi.



 





Asema mambo ya kutegemea wahisani yamepitwa na wakati
WAZIRI Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka Watanzania kushirikiana na Serikali katika kutunza na kuhudumia vituo vya watoto wenye mahitaji maalumu na wasiojiweza badala ya kutegemea wahisani kutoka nje kwani mambo hayo yamepitwa na wakati.

Ametoa kauli hiyo leo Jumapili, Juni 21, 2026 katika harambee ya uchangiaji wa jengo la kitega uchumi cha kanisa la Anglika jijini Dodoma. “Mambo ya misaada yamepitwa na wakati na hata katika bajeti Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameendelea kusisitiza kuwa na bajeti ya nchi ambayo inategemea rasilimali za ndani ya nchi”.

Pia, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu ametoa rai halmashauri zote nchini ziandae orodha ya vituo vya kulelea watoto wenye mahitaji maalumu na wasiojiweza na kuona namna ya kuvisaidia ambapo amesisitiza si vema kuwaandikia watu hao barua za kwenda kuomba misaada pindi wanapofika kwenye ofisi za umma.

Waziri Mkuu amesema awali katika maeneo mbalimbali nchini ilizoeleka kuwa vituo vya kulelea watoto yatima na wenye mahitaji maalumu viliendeshwa kupitia misaada kutoka nje ya nchi dhana ambayo watu wanatakiwa kuachana nayo.

Kadhalika, Waziri Mkuu ametumia fursa hiyo kuwahimiza Watanzania kuendelea kusimama katika mafundisho mbalimbali yanayotolewa na viongozi wa dini ikiwemo kuendeleza amani na umoja wa kitaifa.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan analipongeza Kanisa la Anglikana Tanzania kwa kuendeleza mradi wa ujenzi wa kitega uchumi kwa sababu ukuaji wa uchumi ni miongoni mwa malengo muhimu ya maendeleo.

Awali, Katibu Mkuu wa Kanisa la Anglikana Tanzania, Kasisi Canon Dkt. George Lawi alisema ili kuimarisha uwezo wa kifedha na kupunguza utegemezi, Kanisa la Anglikana Tanzania lilianzisha mradi wa kitega uchumi jijini Dodoma na kuhakikisha linakuwa na vyanzo endelevu vya mapato vitakavyowezesha utekelezaji wa majukumu ya kiroho na kijamii kwa ufanisi zaidi.

Alisema jengo hilo linatarajiwa kutoa huduma mbalimbali zikiwezo za hoteli, ofisi na hivyo kuchangia katika kukuza uchumi wa kanisa na Taifa kwa ujumla. “Mradi huu umefikia hatua ya umaliziaji na umeshagharimu shilingi bilioni tatu na bado zinahitajika shilingi bilioni 1.5 ili kukamilisha na ndiyo sababu ya kufanya harambee leo.”

Pia, Dkt. Lawi alitumia fursa hiyo kumuahidi Waziri Mkuu kuwa Kanisa Anglikana Tanzania litaendelea kuwa mshirika wa Serikali katika juhudi za kuwaletea wananchi maendeleo endelevu kupitia sekta za elimu, afya, uwezeshaji wa jamii na kukuza maadili mema.

Katika harambee hiyo zaidi ya shilingi bilioni moja zilipatikana, ambapo pia Kanisa Anglikana limempa Heshima ya Kikanisa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa Lay Canon, mshauri wa mambo ya Kanisa baada ya kuridhishwa na utendaji wake.




 





Na Oscar Assenga,TANGA.

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Wazo Michael Mwang’onda, amepongeza utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa miundombinu ya kuboresha upatikanaji wa maji safi katika eneo la Mzizima hadi Mikocheni, akisema unadhihirisha dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kusogeza huduma muhimu karibu na wananchi.

Mwenge wa Uhuru 2026 umetembelea na kukagua mradi huo unaotekelezwa na Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Tanga (Tanga UWASA) katika Kata ya Mzizima, ambapo viongozi wa mbio hizo walieleza kuridhishwa na kasi ya utekelezaji wake.


Akizungumza baada ya ukaguzi huo na kushiriki katika zoezi la kumuunganishia mteja mpya huduma ya maji safi, Mwang’onda alisema Serikali chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kutekeleza mkakati wa kuboresha huduma za maji nchini ili kumtua mama ndoo kichwani.

Alisema dhamira hiyo inaonekana kupitia miradi mbalimbali ya kimkakati inayotekelezwa katika sekta ya maji nchini, huku akiipongeza Tanga UWASA kwa usimamizi mzuri wa mradi huo ambao unalenga kuongeza upatikanaji wa huduma ya maji kwa wananchi.

Kwa upande wake, Msimamizi wa Mradi, Mhandisi Aaron Chanimbaga, akisoma taarifa ya utekelezaji alisema mradi huo wenye thamani ya Shilingi milioni 233.4 umefikia asilimia 50 ya utekelezaji.

Alieleza kuwa mradi huo unatarajiwa kukamilika ifikapo Septemba mwaka huu na unalenga kunufaisha zaidi ya wananchi 4,780 kwa kuwapatia huduma ya maji safi na salama kwa uhakika.

Mbio za Mwenge wa Uhuru 2026 zinaongozwa na kauli mbiu isemayo: “Tanzania ni yetu sote, tushirikiane kwa pamoja kuleta maendeleo.”









Top News