Katibu wa NEC – Uchumi na Fedha wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Jamal Kassim Ali, leo tarehe 6 Septemba 2026 amezindua rasmi mradi wa vibanda vya biashara kwa wajasiriamali wadogo unaomilikiwa na CCM Mkoa wa Kagera, mjini Bukoba.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa mradi huo, Ndugu Jamal ameipongeza CCM Mkoa wa Kagera kwa kutumia rasilimali za Chama kuanzisha mradi wenye tija, unaolenga kuchochea shughuli za kiuchumi, kuwawezesha wajasiriamali wadogo na kuongeza uwezo wa Chama katika kujitegemea.

Amesema wajasiriamali wadogo wa leo ndio msingi wa wawekezaji wakubwa wa kesho, hivyo amewataka viongozi, hususan madiwani, kutambua na kutumia fursa za kiuchumi zilizopo katika kata zao ili kuwawezesha vijana kujiajiri na kujenga uchumi wa maeneo yao.

Aidha, Ndugu Jamal amewataka wanachama wa CCM kuishi kwa vitendo Imani na misingi ya Chama, akisisitiza umuhimu wa nidhamu, usawa na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu ya Chama.

Amesema hakuna mwanachama aliye juu ya Chama, na kwamba kila mwanachama anapaswa kuheshimu Katiba, kanuni na taratibu za CCM bila kujali nafasi au cheo alichonacho.

“Hakuna mtu aliye juu ya CCM; wanachama wote ni sawa mbele ya Katiba, kanuni na taratibu za Chama.”







▪️︎ Atoa rai kwa Watanzania kuchukua tahadhari dhidi ya mafuriko

▪️︎ Aagiza ndani ya Septemba kutangazwa zabuni ya ujenzi wa barabara km 11 za Igauri–Ilongero

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, ametoa wito kwa Watanzania na viongozi katika ngazi zote kuchukua tahadhari na kujiandaa mapema kukabiliana na athari zinazoweza kujitokeza kutokana na mvua kubwa zinazohusishwa na hali ya El Niño.

Dkt. Mwigulu ametoa rai hiyo leo, Jumapili, Septemba 06, 2026, wakati akizungumza na wananchi wa Jimbo la Ilongero, Wilaya ya Singida, mkoani Singida, katika ziara yake ya kikazi ya kusikiliza kero za wananchi na kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Amesema maeneo yenye historia ya mafuriko yanapaswa kutambuliwa mapema na hatua za tahadhari kuchukuliwa, huku akiwataka wananchi wanaoishi katika maeneo hatarishi kuzingatia taarifa na maelekezo ya mamlaka husika.

“Maeneo ambayo mnaona ni ya hatari sana Watanzania tunayajua. Tunayajua maeneo yenye historia ya mafuriko. Ni vyema tukaanza kuchukua tahadhari kwa sababu hicho ndicho tunachoweza kukifanya,” alisema.

Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea kuimarisha uwezo wa kukabiliana na athari za mvua, ikiwemo kuwa na magari ya kuchimba mabwawa katika kila ukanda, huku akisisitiza kuwa wananchi wanapaswa kuepuka kujenga au kuishi katika maeneo yanayofahamika kuwa hatarishi kwa mafuriko.

Kuhusu barabara ya Igauri–Ilongero, Dkt. Mwigulu ametoa agizo la kuhakikisha ndani ya mwezi huu mchakato wa kumpata mkandarasi wa ujenzi wa kilomita 11 za awali unakamilika.

“Ndani ya mwezi huu huu, muwe mmeshatangaza kupata mkandarasi wa kuanza kujenga hizi kilomita 11 za awali ambazo zitaziba hili pengo kuanzia hapa mpaka kwenye lami na kupita kidogo mji wa Ilongero,” alisema.

Alisema fedha kwa ajili ya mradi huo zipo na kinachosubiriwa ni kumpata mkandarasi, akisisitiza kuwa ujenzi huo unapaswa kuanza haraka.

Dkt. Mwigulu pia amesisitiza umuhimu wa Serikali kubana matumizi yasiyo ya lazima na kuelekeza fedha zinazookolewa kwenye maeneo yenye kipaumbele, hususan elimu, afya, maji na miundombinu.

Amesema hatua hiyo ni muhimu kutokana na ongezeko kubwa la wanafunzi wanaotarajiwa kuingia kidato cha kwanza kuanzia mwaka 2028, hivyo Serikali inapaswa kuanza mapema maandalizi ya madarasa, maabara, maktaba na mahitaji mengine ya elimu.

“Ni fedha ya Serikali, ni fedha ya walipa kodi wa Tanzania, ni fedha ambayo inaweza kwenda kutatua hizi changamoto watoto wasikae chini,” alisema.

Kuhusu afya, Waziri Mkuu amesisitiza kuwa ambulensi zinapaswa kuwa tayari muda wote na kuwa na mafuta ili wagonjwa wanaohitaji huduma za dharura na rufaa wasicheleweshwe.

“Ambulensi zetu ziwe standby. Tulishanunua magari, yawe na mafuta. Kila wakati yawe na mafuta. Tusichangishe wagonjwa kuweka mafuta kwenye gari ya Serikali kubeba mgonjwa ambaye yuko mautini,” alisema.

Aidha, ametoa wito kwa Watanzania kujiunga na Bima ya Afya kwa Wote, akisema mfumo huo ni suluhisho la kudumu la kupunguza utegemezi wa michango ya dharura wakati wananchi wanapokabiliwa na gharama za matibabu.

“Watanzania wote tuingie kwenye bima ya afya. Tutaepukana na matatizo mengi sana ambayo tumeyatafutia majawabu ya dharura, lakini yanahitaji yapate majawabu ya kudumu,” alisema.

Kuhusu maji, Dkt. Mwigulu amesema Serikali itaendelea kutekeleza miradi ya maji na umwagiliaji kwa ushirikiano wa wizara zinazohusika, ili miradi hiyo iweze kunufaisha wananchi, mifugo na shughuli za uzalishaji.

Amesema Serikali itaendelea kusimamia matumizi yenye tija ya rasilimali za umma na kuhakikisha miradi ya maendeleo inatekelezwa kwa kuzingatia thamani ya fedha, ufanisi na mahitaji halisi ya wananchi.











Na, Mwandishi Wetu -Dodoma

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuzindua majengo ya Ofisi za Wizara, Taasisi za Serikali pamoja na barabara za lami zenye urefu wa kilomita 57.1 katika Mji wa Serikali Mtumba,Jijini Dodoma.

Uzinduzi huo unatarajiwa kufanyika jumanne Septemba nane mwaka huu katika Uwanja wa Mashujaa uliopo ndani ya Mji wa Serikali Mtumba.

Hayo yamebainishwa Jijini Dodoma leo (06 Septemba, 2026) na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Mhe.Profesa Palamagamba Kabudi, wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maandalizi ya hafla hiyo.

Alisema uzinduzi huo utahusisha maeneo matatu makuu ambayo ni majengo ya Ofisi za Wizara 26, Taasisi 11 za Serikali na barabara za lami zenye urefu wa kilomita 57.1.

Profesa Kabudi alisema kukamilika kwa majengo hayo, kutawezesha watumishi 18,510 kutumia ofisi za Mji wa Serikali, Mtumba.

“Ujenzi wa Mji wa Serikali Mtumba ulianza kutekelezwa kwa awamu, ambapo awamu ya kwanza ilihusisha ujenzi wa majengo 23 ya Ofisi za muda.ujenzi wa majengo hayo ulianza Novemba 28 mwaka 2018 na kukamilika Machi 22 mwaka 2019, hatua iliyowezesha baadhi ya watumishi wa Wizara na taasisi kuanza kuhamia.

Aliongeza kuwa :” Awamu ya pili ya ujenzi ilianza Oktoba, 2021, ikiwa inalenga kujenga majengo ya kudumu kwa ajili ya watumishi wote wa Wizara na Taasisi zilizopangwa kuhamia Mtumba.Pia ilihusisha ujenzi wa miundombinu na huduma mbalimbali za kijamii, ikiwemo barabara za lami.

Profesa Kabudi alisema mbali na barabara hizo, miundombinu ya kudumu ya mawasiliano pamoja na Uwanja wa Mashujaa imekamilika na itakuwa sehemu ya miundombinu itakayotumika katika shughuli za Serikali.

Hata hivyo, alisema baadhi ya miradi bado iko katika hatua mbalimbali za utekelezaji, ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya umeme inayopita chini ya ardhi yenye urefu wa kilomita 42.

“Kazi ya ujenzi wa miundombinu ya maji safi na uondoshaji wa maji taka, TEHAMA, ufungaji wa mifumo ya usalama ya CCTV Camera, ujenzi wa kituo cha zimamoto pamoja na utekelezaji wa mpango wa upandaji miti na ustawishaji wa Mji wa Serikali nazo zinafanyika, "alisema.

Alisema Rais Dkt.Samia ameendelea kuweka msisitizo katika kuboresha mazingira hayo, ikiwa ni pamoja na kutoa fedha kwa ajili ya ununuzi wa samani za Wizara na taasisi 26 zinazohamia katika majengo hayo.

Profesa Kabudi alisema hatua hizo zinaendelea kuifanya Mji wa Serikali Mtumba kuwa miongoni mwa alama muhimu za utekelezaji wa dhana ya Dodoma kuwa kitovu cha shughuli za Serikali.

Alisema uwekezaji huo pia unatarajiwa kuongeza fursa za kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa Dodoma na Tanzania kwa ujumla.






Benki ya Exim Tanzania inaadhimisha miaka 29 tangu kuanzishwa kwake chini ya kaulimbiu "Miaka 29 ya Ubora kwa Vitendo," ikisherehekea karibu miongo mitatu ya ukuaji, uhusiano na wateja, ushirikiano na mchango kwa jamii inazozihudumia.

Mwaka 1997, Benki ya Exim Tanzania ilianza safari yake ikiwa na idadi ndogo ya wateja, na hatua kwa hatua ikajenga uwepo wake katika soko la Tanzania. Kwa kipindi cha miaka 29, Benki imekua na kuwa mojawapo ya taasisi za kifedha zinazoongoza nchini Tanzania, ikitambulika kwa ubunifu wake, suluhisho zinazomlenga mteja na mchango wake mkubwa katika ukuaji wa kiuchumi wa nchi, ikiwa na zaidi ya matawi 30 nchini kote na uwepo nje ya Tanzania katika masoko ya Comoro, Djibouti, Uganda na Ethiopia.

Kama sehemu ya safari hii, Benki ya Exim ilikuwa benki ya kwanza ya Tanzania kufungua matawi nje ya nchi, na kuifanya kuwa mojawapo ya benki chache za Tanzania zilizofanikiwa kupanua shughuli zake nje ya mipaka ya taifa hili. Kupitia mtandao wake mpana wa matawi na mifumo ya kisasa ya kibenki ya kidijitali, Benki inaendelea kuwawezesha watu binafsi na wafanyabiashara kwa suluhisho za kifedha zenye kutegemewa, nyumbufu na zinazolenga mustakabali, ikithibitisha dhamira yake ya kuchochea ukuaji endelevu na ustawi katika ukanda huu.

Safari ya Benki hii, hata hivyo, imekwenda mbali zaidi ya kutoa huduma za kifedha. Kwa miaka mingi, Benki ya Exim imewekeza katika mipango inayochangia ustawi na maendeleo ya jamii kupitia jukwaa lake la Exim Cares, likiwa na programu zinazogusa afya, elimu, ustawi wa vijana, uwezeshaji wa wanawake na uhifadhi wa mazingira. Mipango hii ni pamoja na msaada wa muda mrefu kwa kampeni za uchangiaji damu, ushirikiano na Young Scientists Tanzania (YST), Women Empowerment Program, pamoja na afua mbalimbali za kusaidia taasisi za afya na uhifadhi wa mazingira.

Mwaka huu, Benki inafanya maadhimisho yake kwa namna tofauti kwa kuupeleka mkondo huo moja kwa moja kwa jamii inazozihudumia. Kama sehemu ya maadhimisho ya miaka 29, Benki ya Exim imekuwa ikifanya shughuli za usafi wa mazingira na kukabidhi vifaa vya usafi katika maeneo mbalimbali kupitia mtandao wake wa matawi, ikiwemo masoko, hospitali na shule katika mikoa mbalimbali, kwa lengo la kuhakikisha kunakuwa na mazingira safi, salama na yenye afya kwa jamii.

Jijini Dar es Salaam, shughuli hizo ni pamoja na ukabidhi wa vifaa vya usafi kwa Manispaa ya Kinondoni na zoezi la usafi wa jamii katika Fukwe ya Kawe, likikutanisha wafanyakazi wa Benki ya Exim, wadau na wanajamii katika kuchangia maeneo safi na yenye afya zaidi.

Akizungumza wakati wa maadhimisho hayo, Mkuu wa Idara ya Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania, Bw. Stanley Kafu, alisema maadhimisho ya miaka 29 yanatoa fursa ya kuwathamini watu na jamii ambazo zimekuwa muhimu katika safari ya Benki, huku ikithibitisha dhamira yake ya kuendelea kuleta thamani zaidi siku zijazo.

"Safari yetu ya miaka 29 imejengwa pamoja na wateja wetu, wafanyakazi, washirika na jamii tunazozihudumia. Kila mteja aliyetuamini, kila biashara tuliyoisaidia na kila ushirikiano tulioujenga umechangia kuifanya Benki ya Exim kuwa taasisi iliyopo leo. Maadhimisho haya kwa hiyo si tu kuhusu kusherehekea Benki ya Exim; ni kuhusu kusherehekea kila mmoja aliyekuwa sehemu ya safari yetu," alisema Bw. Kafu.

Aliongeza kuwa uamuzi wa kuadhimisha maadhimisho hayo kupitia shughuli za kijamii unaakisi imani ya Benki kwamba dhamira yake inakwenda mbali zaidi ya huduma za kifedha.

"Tunafanya maadhimisho kwa namna tofauti mwaka huu kwa kuubadilisha mkondo huu kuwa kitu chenye maana kwa jamii zinazotuzunguka. Usafi wa mazingira ni jukumu la pamoja, na kupitia shughuli hizi na ukabidhi wa vifaa vya usafi, tunachangia kwa vitendo huku tukihamasisha watu wengi zaidi kumiliki maeneo tunayoyashiriki sote. Hii ndiyo maana halisi ya Ubora kwa Vitendo, kubadilisha dhamira kuwa hatua za vitendo zenye thamani kwa jamii zinazotuzunguka," alisema.

Akizungumza kwa niaba ya jamii, Diwani wa Kata ya Kawe, Bw. Benard Fabian Malima, alipongeza Benki ya Exim kwa kuchagua Kawe kama mojawapo ya maeneo ya shughuli zake za maadhimisho.

"Kwa niaba ya wakazi wa Kawe, napenda kuishukuru Benki ya Exim kwa mpango huu. Fukwe ya Kawe ni eneo linalotumiwa na watu wengi katika jamii hii kila siku, na kuliweka safi ni jambo linalonufaisha sote. Ukabidhi wa vifaa vya usafi kwa Halmashauri yetu utasaidia sana jitihada zetu za kuendelea kuweka mazingira safi, na tunatarajia taasisi nyingine zaidi zitafuata mfano huu," alisema Bw. Malima.

Shughuli hizo za kijamii zilifanyika katika maeneo mbalimbali kupitia mtandao wa Benki ya Exim, zikiwawezesha wafanyakazi na wadau katika jamii mbalimbali kushiriki katika mpango huu wa maadhimisho.

Aidha, Benki ya Exim inapoelekea mwaka wake wa 30, inaendelea kuwa na dhamira ya kujenga juu ya safari yake ya miaka 29 kwa kuendelea kubuni, kuboresha uzoefu wa wateja, kusaidia biashara na kuleta thamani zaidi kwa wateja wake, wadau na jamii.
Mkuu wa Kitengo cha Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania Stanley Kafu (wa pili kulia) wakipeana mikono na Diwani wa Kata ya Kawe Mheshimiwa Fabian Malima (katikati) baada ya kukabidhi vifaa vya kufanyia usafi wa jiji. Shughuli hiyo imefanyika kama kilele cha kusherehekea miaka 29 ya Benki ya Exim toka uanzishwaji wake nchini ambapo, walishiriki pia katika usafi wa fukwe za bahari katika maeneo ya Kawe. Tukio hilo limefanyika  tarehe 5 Septemba 2026, jijini Dar es salaam na kushuhudiwa na Meneja Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania, Kauthar D'souza (kulia), Mkuu wa Kituo cha Polisi Kawe ASP Ally Liviga (kushoto) na Afisa Usafishaji Manispaa ya Kinondoni Alban Mugyabuso wa pili Kulia.





Uongozi wa Mamlaka ya Hifadhi ya eneo la Ngorongoro (NCAA) umeeleza kuwa, umedhamiria kuendelea kuboresha utoaji huduma kwa watalii kwa njia za kisasa kupitia matumizi ya teknolojia ya habari na mawasiliano ili kuongeza ufanisi na kasi ya utendaji kazi na ukusanyaji wa mapato.

Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa uhifadhi anayesimamia huduma za Utalii na Masoko Mariam Kobelo ameeleza kuwa lengo la kufanya kazi kidigitali ni kuhakikisha kuwa watoa huduma katika sekta ya utalii wanatumia muda mfupi kuingia na kutoka ndani ya hifadhi pamoja na kuhakikisha maduhuli ya serikali yanakusanywa kikamilifu na kuimarisha usalama wa hifadhi na rasilimali zilizopo.

“Siku mbili zilizopita tumekuwa na changamoto ndogo ndogo katika lango kuu la Ladoure ,tunaendelea kuzitatua kwa ushirikiano mkubwa na wadau wetu”,amesema bi.Kobelo.

Amewashukuru waongoza watalii wote na wadau katika sekta hiyo kwa kuonesha ushirikiano wa kutosha katika kufanikisha maboresho hayo.

Ameongeza kuwa mteja yeyote atakayekutana na changamoto za kiutendaji katika kipindi hiki ni vema akawasiliana na maafisa wa mamlaka hiyo ambao wapo katika lango hilo na maeneo mengine na watasaidiwa ili waweze kuendelea na safari zao kwa muda kama walivyopanga.

Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro katika mwelekeo wa utendaji wake mpya imedhamiria kuimarisha shughuli zake za kutoa huduma bora kwa watalii katika viwango vya kimataifa na kuendelea kuimarisha dawati la huduma na ukarimu kwa wateja.










Serikali imeutaka Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) kujipanga kikamilifu katika maandalizi ya mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027, hususan katika kuhakikisha wageni watakaofika nchini wanapata huduma bora za matibabu bila vikwazo.

Agizo hilo limetolewa l na Naibu Waziri wa Afya Mhe. Dkt. Florence Samizi (Mb.) ambaye amesema NHIF ina jukumu muhimu la kuratibu suala la bima ya afya wakati wa mashindano hayo ili kuhakikisha wageni wanapata huduma za matibabu kwa urahisi pindi wanapohitaji huduma hizo.

“Tuwape uhakika wa huduma bora ili waone fahari kuwapo hapa nchini katika kipindi chote cha mashindano hayo,” amesema Dkt. Samizi.

Amesema maandalizi ya huduma za matibabu yanapaswa kuzingatia pia huduma za dharura pamoja na huduma maalum, ikiwemo za moyo na mifupa, ili kukidhi mahitaji mbalimbali ya afya yatakayoweza kujitokeza wakati wa mashindano.

Aidha alidokeza kuwa tayari Wataalamu kutoka Shirikisho la Soka Afrika (CAF) wamekagua Vituo vya kutolea huduma kwa alengo la kujiridhisha na wamefurahishwa na utayari unaoonyeshwa katika maandalizi ya huduma za matibabu jambo linaloonesha kuwa Tanzania inajiandaa kuhakikisha AFCON 2027 inafanyika katika mazingira salama na yenye huduma bora.

Ameitaka NHIF kushirikiana kwa karibu na Wizara ya Afya, vituo vya kutolea huduma na wadau wengine kuhakikisha mfumo wa huduma za matibabu wakati wa mashindano hayo unakuwa imara, unaopatikana kwa wakati na unaokidhi viwango vinavyohitajika.

Akizungumzia hilo Mkurugenzi Mkuu waa NHIF, Dkt. Irene Isaka alisema kuwa tayari Mfuko umeshajipanga na umeandaa kifurushi maalumu kwa ajili ya wageni wote watakaokuja nchini kwa ajili ya mashindano hayo.

“Tayari tumejipanga na tuna kifurushi ambacho tutakileta Wizarani ili tupate baraka ya Wizara hivyo tunashukuru sana kwa maelekezo haya ambayo yanaboresha na kuhakikisha tunajipanga vyema,” alisema Dkt. Isaka. ‎


‎ ‎ ‎NAIBU Waziri wa Afya, Mhe Dkt. Florence George Samizi (Mb), amelipongeza Baraza la Wafanyakazi la Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) kwa kuwa moja ya mabaraza bora nchini. Amelitaka baraza kuhakikisha ajenda ya Bima ya Afya kwa wote inawafikia wananchi wengi zaidi.

Nimefurahi kusikia kwamba katika kipindi cha mwaka wa fedha 2025/2026 Mfuko umeweza kufikia 10.7% ya Wananchi toka 8% ya wananchi iliyodumu kwa takriban miaka 10. Pamoja na pongezi hizo Mh. NAIBU WAZIRI ameutaka Mfuko kutumia TEHAMA na kusajili wanachama wengi zaidi ili kutimiza ahadi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwafikishia wananchi wote huduma za bima ya afya. Hii itasaidia wananchi kuondokana na umaskini pale wanapopata maradhi. ‎

 ‎Dkt. Samizi ametoa maelekezo Hayo wakati wa mkutano wa nne wa wa Baraza la 4 wafanyakazi NHIF, Jijini Arusha, na kusisistiza menejimenti ya wafanyakazi wa NHIF kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia uadilifu, weledi na uwajibikaji, huku wakisikiliza na kutatua kwa wakati kero za wananchi. 

‎ ‎Aidha, amesisitiza umuhimu wa kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kuwa na bima ya afya. Kutoa huduma bora na kuwa na mfumo wa kupokea mrejesho toka kwa wananchi. ‎ ‎Katika kuelekea maadhimisho ya miaka 25 tangu kuanzishwa kwa NHIF, Dkt. Samizi amesema ni muhimu mfuko huo kuonesha mafanikio yaliyopatikana. 

Kuwepo kwa NHIF kumesaidia kuboresha huduma za Afya kwa kulipa madai na kutoa mikopo kwa vituo vya afya. Ni vema wanachi wakajulishwa hatua kubwa iliyofikiwa katika huduma za Afya na mchango wa NHIFkatika Sekta hii muhimu. 

Mlianza na vituo vichache sana mwaka 2001 hivi sasa yaani mwaka wa Fedha 2025/26 mmesajili zaidi ya vituo 10,600 nchi nzima. Ni vema kuonesha namna mlivyokabiliana na changamoto za wakati ule na namna zilivyowasaidia kuboresha Mfuko katika utoaji wa huduma. ‎ 

‎Amesema mafanikio hayo yanadhihirishwa na kujituma, ushirikiano, umoja na mshikamano miongoni mwa watumishi wa NHIF ili kufikia malengo ya mfuko kwa lengo la kutekeleza jitihada za Serikali za kuhakikisha wananchi wanapata bima ya Afya. ‎

 ‎Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, Dkt. Irene Isaka, ameeleza mafanikio yaliyopatikana ikiwa ni pamoja na kupunguza muda wa kilipa madai toka zaidi ya siku 90 hadi wastan wa siku 50 kwa mwaka wa Fedha 2025/2026. Vile vile alieleza kwamba Mfuko umeendelea kuimarika ambapo ziada imeongezeka kwa 57% Mfuko umepunguza matumizi kwa asilimia13% na uwekezaji umeongezeka kwa 106%.

Hii imewezesha Mfuko kuendeleza kifurushi cha wanafunzi, Toto Afya. Mfuko kusajili kifurushi cha tarangire, Mikumi, Ngorongoro, Serengeti Tanzanite na kifurushi cha vikundi yaani Umoja Afya ambacho ni sh. 60, 000 kwa matibabu ya mwaka mzima.

Vile vile alielezea mikakati inayotekelezwa na mfuko huo katika kufikia malengo yake ikiwa ni pamoja na matumizi ya TEHAMA kwenye usajili, uchakataji madai na kupambana na udanganyifu.

 Mfuko pia unashirikisha Sekta Binafsi katika usajili wa wanachama na katika huduma za matibabu. ‎ ‎Mwakilishi wa chama Cha wafanyakazi TUGHE, Bw.Paul wamepongeza baraza Hilo kuzingati misingi ya Kazi stahiki za wafanyakazi kwenye taasisi hiyo. ‎

 ‎Baadhi ya wafanyakazi walioshiriki semina elekezi ya siku mbili wamesema wamepata maarifa na mwelekeo mpya ambao utawasaidia kuboresha utendaji wao wa kazi na utoaji wa huduma kwa wananchi.

‎ Bima ya Afya kwa wote! Jiunge sasa!
Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Ndg. Abdi Mahmoud Abdi, amesema uwepo wa maskani za vijana wa CCM ni miongoni mwa njia muhimu za kuimarisha umoja na mshikamano miongoni mwa wanachama na viongozi wa chama katika ngazi mbalimbali.

Ndg. Abdi ameyasema hayo wakati wa ufunguzi wa Maskani ya CCM ya Kibweni Shaba Juu, iliyopo katika Jimbo la Mkwajuni, Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Amesema maskani zina nafasi muhimu katika kuwakutanisha wanachama, hususan vijana, na kuwawezesha kubadilishana mawazo, kujenga na kuimarisha mahusiano, pamoja na kushirikiana katika shughuli mbalimbali za maendeleo na za chama.

Aidha, Ndg. Abdi amewataka wana-CCM na wanamaskani kuendelea kudumisha umoja na mshikamano uliopo nchini, sambamba na kuunga mkono juhudi zinazofanywa na viongozi wakuu wa nchi na chama katika kuwaletea wananchi maendeleo.

Amesisitiza kuwa umoja, mshikamano na ushirikiano ni msingi muhimu katika kuendelea kuijenga CCM imara, yenye uwezo wa kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kwa manufaa ya wananchi.











Top News