Benki ya Absa Tanzania, kwa kushirikiana na GirlCode, shirika lisilo la kiserikali lenye makao yake nchini Afrika Kusini linalolenga kuwawezesha wasichana kutoka mazingira yenye changamoto kwa kuwapatia ujuzi na rasilimali za kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika sekta ya teknolojia, imetangaza kurejea kwa mashindano ya GirlCode Tanzania Hackathon kwa mwaka wa pili mfululizo.

Hatua hiyo inafuatia mafanikio makubwa yaliyopatikana mwaka 2025, ambapo timu ya Tanzania iliibuka na tuzo kuu ya Pan-African Grand Prize yenye thamani ya Dola za Marekani 5,000.

GirlCode Hackathon ni sehemu ya mpango mpana wa GirlCode unaolenga kuwawezesha wanawake vijana barani Afrika kwa kuwapatia ujuzi wa vitendo katika teknolojia, kuwaunganisha na walezi na wataalamu kupitia programu za ushauri, pamoja na kuwapa fursa ya kubuni suluhisho zinazolenga kukabiliana na changamoto halisi katika jamii zao.

Kurudi kwa mashindano hayo nchini Tanzania kunatajwa kuwa hatua muhimu katika kuimarisha kizazi cha wataalamu wanawake katika teknolojia na kujenga juu ya mafanikio yaliyopatikana na washiriki wa Tanzania mwaka jana.

Ushindi wa Tanzania mwaka 2025 ulidhihirisha umuhimu wa kuwekeza kwa wanawake vijana kama wabunifu, wajenzi wa suluhisho na watatuzi wa changamoto. Mafanikio hayo hayakuweka tu Tanzania katika ramani ya GirlCode Hackathon barani Afrika, bali pia yalitoa hamasa kwa wanawake vijana zaidi nchini kujiona kuwa sehemu ya uchumi wa kidijitali unaokua barani Afrika.

Akizungumzia kurejea kwa mpango huo nchini Tanzania, Ofisa Mtendaji Mkuu wa GirlCode, Zandile Mkwanazi, alisema shirika hilo linajivunia mafanikio yaliyopatikana na timu ya Tanzania mwaka jana.

“GirlCode inajivunia sana kile ambacho timu ya Tanzania ilifanikiwa kukipata mwaka jana. Kushinda tuzo kuu ya Pan-African Grand Prize kumeonyesha kiwango cha vipaji, ubunifu na uwezo uliopo miongoni mwa wanawake vijana nchini Tanzania,” alisema.

Aliongeza kuwa kurejea kwa mashindano hayo kwa mwaka wa pili kunalenga kujenga juu ya mafanikio yaliyopatikana na kuwapa wanawake vijana zaidi fursa ya kuendeleza ujuzi wao, kufanya kazi kwa pamoja na kubuni suluhisho zinazotumia teknolojia na ambazo zinaweza kuwa na matokeo chanya katika jamii.

Hackathon ya mwaka huu itawakutanisha wanafunzi wa kike, wahitimu, wanaotarajia kuwa watengenezaji wa programu pamoja na wabunifu vijana, ambao watashirikiana katika timu, kupata ushauri kutoka kwa wataalamu na kuwasilisha suluhisho zao mbele ya jopo la majaji.

Washiriki watatakiwa kutumia fikra tunduizi, kutumia ujuzi wao wa kiteknolojia na kubuni mawazo mapya yanayoweza kuchangia katika mustakabali wa ajira, ujasiriamali na mageuzi ya kidijitali.

Mbali na mashindano, mpango huo utatoa jukwaa muhimu kwa wanawake vijana kupata uzoefu na uelewa zaidi kuhusu sekta ya teknolojia, kuunganishwa na wenzao pamoja na washauri, na kujenga kujiamini katika kutafuta ajira na fursa mbalimbali katika sekta hiyo.

Kwa washiriki wengi, uzoefu huo unaweza kuwa hatua ya kuingia katika programu za mafunzo kwa vitendo, ajira, ujasiriamali na kuendelea kujifunza katika teknolojia.

Akizungumzia umuhimu wa mpango huo, Ofisa Mkuu wa Uendeshaji wa Benki ya Absa Tanzania, Oscar Mwamfwagasi, alisema ushiriki wa waanzilishi wa biashara ndogo na za kati (SMEs) ni moja ya mambo yanayoongeza thamani katika Hackathon ya mwaka huu.

“Kinachofanya Hackathon ya mwaka huu kuwa na thamani zaidi ni ushiriki wa moja kwa moja wa waanzilishi wa biashara ndogo na za kati, ambao wanaleta uzoefu wa vitendo katika biashara pamoja na changamoto halisi zinazokabili biashara kwenye programu hii.”

Alisema ushiriki wao unasaidia kuboresha safari ya kujifunza kwa washiriki, huku ukifungua fursa kwa kampuni changa kuonyesha mawazo yao, kupata mwongozo kutoka kwa wataalamu wa sekta mbalimbali na kujenga mahusiano yanayoweza kusaidia kuharakisha ukuaji wa biashara zao.

“Programu kama hii ni muhimu katika kukuza ubunifu, kuwawezesha wajasiriamali na kujenga mfumo jumuishi zaidi wa kidijitali unaosaidia maendeleo endelevu ya Afrika,” alisema Mwamfwagasi.

Kadiri GirlCode Hackathon inavyoendelea kukua katika mataifa mbalimbali ya Afrika, Tanzania imeendelea kuwa mfano wa kile kinachoweza kufikiwa pale wanawake vijana wanapopewa majukwaa, rasilimali na mitandao sahihi ya kuwawezesha.

Ushindi wa Tanzania katika mashindano ya Pan-African mwaka 2025 umeweka msingi imara, huku toleo la mwaka huu likilenga kutoa hamasa kwa kizazi kijacho cha wanawake wa Tanzania wanaotaka kujikita katika teknolojia kufikia mafanikio makubwa zaidi.

GirlCode imewahimiza wanawake vijana nchini Tanzania, wadau, walezi na washiriki wa mfumo wa teknolojia kuunga mkono Hackathon ya mwaka huu na kushirikiana katika kujenga mustakabali wa kidijitali unaojumuisha watu wengi zaidi barani Afrika.

GirlCode Tanzania Hackathon 2026 itafanyika tarehe 26–27 Septemba 2026.

Maombi ya ushiriki: https://www.girlcode.co.za/hackathon-2026



Na Julitha Mlay ,NATCOM
KATIBU Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo, ametembelea Banda la Tume ya Taifa ya UNESCO ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika maadhimisho ya Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu Kitaifa yanayoendelea jijini Tanga.

Katika ziara hiyo, Prof. Nombo alipata fursa ya kujionea shughuli mbalimbali zinazofanywa na Tume hiyo, pamoja na maudhui yanayotolewa kwa umma kuhusu UNESCO, majukumu ya Tume na programu zake katika maeneo ya elimu, sayansi, utamaduni, mawasiliano na taarifa.

Prof. Nombo aliambatana na Mkurugenzi wa Elimu ya Ufundi, Dkt. Fredrick Salukele, ambapo walipata maelezo kuhusu namna Tume inavyotumia majukwaa ya kitaifa kuwafikia wananchi, wanafunzi, walimu, vijana na wadau mbalimbali kwa kuwapatia taarifa kuhusu UNESCO na fursa zinazopatikana kupitia programu zake.

Ushiriki wa Tume ya Taifa ya UNESCO katika Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu Kitaifa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha uelewa wa umma kuhusu UNESCO, pamoja na kuonesha mchango wa elimu, sayansi, utamaduni, mawasiliano na taarifa katika kukuza maarifa, ubunifu na maendeleo endelevu nchini.

Kupitia maonesho hayo, Tume inaendelea kuwafikishia wananchi taarifa kuhusu kazi za UNESCO na maeneo mbalimbali yanayohusiana na utekelezaji wa programu zake nchini Tanzania, huku ikihamasisha jamii kutumia maarifa na fursa zilizopo kwa maendeleo ya mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.

Maadhimisho ya Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu Kitaifa yanaendelea jijini Tanga yakishirikisha taasisi na wadau mbalimbali wa sekta ya elimu, ujuzi na ubunifu, kwa lengo la kuelimisha jamii kuhusu fursa, huduma na jitihada zinazochangia maendeleo ya rasilimali watu nchini




MWANAFUNZI wa Kidato cha Tatu katika Shule ya Ufundi Tanga, Neema Bundala akionesha uwezo wake wa kujua mfumo wa nchini unafavyofanya kazi kwenye Banda la NACTVET ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea katika  katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara, jijini Tanga.

Na Mwandishi Wetu, Tanga
MWANAFUNZI wa Kidato cha Tatu katika Shule ya Ufundi Tanga, Neema Bundala, amesema mkondo wa Amali katika shule za sekondari unawajengea wanafunzi ujuzi unaowawezesha kujiajiri mara baada ya kumaliza masomo, huku wakisubiri matokeo ya mitihani ya Taifa.

Neema ameyasema hayo wakati akizungumza katika Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea katika Banda la Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET), katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara, jijini Tanga

Amesema anasoma fani ya Ufundi wa Magari (Motor Vehicle Mechanics), ambapo mafunzo hayo yanamwezesha kupata ujuzi wa vitendo utakaomsaidia kuanza kujiajiri mara baada ya kuhitimu.

“Kwa mfano mimi nasoma Ufundi wa Magari, hivyo ninapohitimu nitakuwa na ujuzi wa kutengeneza magari na ninaweza kuanza kujiajiri na nikisoma Kidato cha Tano na cha Sita, nitakuwa nimeongeza umahiri na nikifika chuo nitakuwa mbobezi zaidi,” amesema Neema.

Amesema mkondo wa Amali ni muhimu kwa wanafunzi wa kike kwa kuwa unawapa fursa ya kujenga uwezo wa kujiajiri na pia kuajirika katika taasisi mbalimbali kutokana na kuwa na ujuzi unaohitajika katika soko la ajira.
MWANAFUNZI wa Chuo cha VETA Tanga , Maria Moshi akizungumza na wananchi waliotembelea  Banda la VETA  kwenye  ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea katika  katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara, jijini Tanga waliotaka kujua mashine ya kutoteleshea vifaranga.


Na Mwandishi Wetu, Tanga
CHUO cha Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) Tanga kimebuni mashine ya kutotoleshea vifaranga yenye uwezo wa kutotolesha vifaranga 840 kwa wakati mmoja, huku mabaki ya maganda ya mayai yakitumika kutengeneza chakula cha kuku.

Akizungumza katika Banda la VETA kwenye Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara jijini Tanga, mwanafunzi wa chuo hicho, Maria Moshi, amesema mashine hiyo inatoa fursa kwa wafugaji na wajasiriamali kupata vifaranga bora na kuendeleza biashara ya kuku.

Amesema mashine hiyo inaambatana na mashine ya kupima na kuchambua mayai kabla ya kuingizwa kwenye mashine ya kutotoleshea, ambapo mayai yasiyofaa hutenganishwa.

Maria amesema mabaki ya maganda ya mayai yanaweza kuchanganywa na virutubisho na kusagwa ili kuzalisha chakula kingine kinachoweza kutumika katika ufugaji wa kuku.

“Kwa mtu anayefanya biashara ya kuku, mashine hii inampa uhakika wa kupata vifaranga vyenye ubora na baadaye kuwauza au kuendeleza ufugaji,” amesema Maria.

Amesema mashine ya kutotoleshea pamoja na mashine saidizi zinauzwa kwa Sh milioni tatu, huku Chuo kikiwa tayari kuzalisha mashine hizo kulingana na mahitaji ya wateja.
WAZIRI wa Uchukuzi Prof. Makame Mbarawa (Mb) akizungumza katika bamda la Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) alipotembelea wakati wa Kongamano la Nne la Kimataifa la Sekta ya Uchukuzi na Usafirishaji, linalofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam

Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) imepongezwa kwa kuendelea kusimamia sekta ya usafiri wa anga kwa ufanisi na kuimarisha utoaji wa huduma kupitia mifumo ya kisasa ya kidijitali.

Pongezi hizo zimetolewa na Waziri wa Uchukuzi Mh. Prof.Makame Mbarawa aliyekuwa mgeni rasmi katika Kongamano la Nne la Kimataifa la Sekta ya Uchukuzi na Usafirishaji, linalofanyika tarehe 20 na 21 Agosti 2026 katika Ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam ambalo TCAA imeshiriki, pindi alipotembelea banda la TCAA.

Mkuu wa Chuo cha Usafiri wa Anga Tanzania (CATC), Aristid Kanje akimuelezea Mhe. Waziri wa Uchukuzi Prof. Makame Mbarawa (Mb) alipotembelea wakati wa Kongamano la Nne la Kimataifa la Sekta ya Uchukuzi na Usafirishaji, linalofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam

Awali akiwa katika banda la TCAA, Prof. Mbarawa alipokewa na Mkuu wa Chuo cha Usafiri wa Anga Tanzania (CATC), Aristid Kanje, kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TCAA Dkt. Jabiri Bakari, ambaye alimweleza kuhusu shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na Mamlaka katika kusimamia na kuendeleza sekta ya usafiri wa anga nchini, ikiwemo matumizi ya teknolojia katika kuboresha utoaji wa huduma.

Kanje pia alimweleza Mh. Waziri kuhusu mfumo wa huduma za kielektroniki unaofahamika kama "Civil Aviation Services Portal (CASP)" unaowawezesha wadau wa usafiri wa anga kupata huduma kwa haraka na kwa ufanisi zaidi, pamoja na Dawati la Huduma kwa Wateja linalowezesha kupokea na kufuatilia maoni na changamoto za wadau.

Kongamano hilo limeandaliwa na Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) na limewakutanisha wadau kutoka sekta ya umma na binafsi kwa ajili ya kubadilishana uzoefu, maarifa na kujadili fursa na changamoto katika sekta ya uchukuzi na usafirishaji nchini.
Afisa Uratibu wa Ukuzaji Mitaala wa VETA Mhandisi Audiface Tarimo akizungumza na waandishi wa habari  katika Banda la VETA kwenye Wiki ya Kitaifa ya Elimu,Ujuzi na Ubunifu linalofanyika Shule ya Sekondari Usagara jijini Tanga.

Na Mwandishi Wetu, Tanga
MAMLAKA ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) inatarajia kuzalisha wataalamu wazawa wapatao 400 katika sekta ya madini baada ya wataalamu wake kwenda nje ya nchi kupata mafunzo na kurejea nchini kwa ajili ya kuwajengea uwezo Watanzania.

Hatua hiyo inalenga kuongeza idadi ya wataalamu wenye ujuzi wa kisasa katika sekta ya madini, ikiwa ni pamoja na kuimarisha ushiriki wa Watanzania katika miradi ya madini na kupunguza utegemezi wa wataalamu kutoka nje ya nchi.

Akizungumza katika Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara jijini Tanga, Afisa Uratibu wa Ukuzaji Mitaala wa VETA, Mhandisi Audiface Tarimo, amesema mamlaka hiyo imezindua mitaala sita ya mafunzo ya uchimbaji wa madini chini ya ardhi kwa ajili ya watanzania kunufaika na rasilimali ya madini.

Tarimo amesema mitaala hiyo imeandaliwa kwa kuzingatia mahitaji ya soko la ajira na matumizi ya teknolojia za kisasa katika sekta ya madini.

Amesema sekta ya madini ni mhimili muhimu wa ukuaji wa uchumi kutokana na mchango wake katika uzalishaji, ajira, mapato ya Serikali na maendeleo ya viwanda, hivyo kuna umuhimu wa kuwa na nguvu kazi yenye ujuzi na weledi unaoendana na mabadiliko ya teknolojia.

“Wataalamu wetu wamekwenda nje ya nchi kujifunza na sasa wamerudi nchini. Kupitia ujuzi huo, tunatarajia kuzalisha Watanzania wapatao 400 watakaokuwa na uwezo wa kufanya kazi katika sekta ya madini,” amesema Tarimo.

Tarimo amesema utekelezaji wa mitaala hiyo ni sehemu ya juhudi za Serikali kuhakikisha Watanzania wanapata nafasi kubwa zaidi katika sekta ya madini kwa kuwa na wataalamu wenye ujuzi unaohitajika katika soko la ajira.

Amesema hatua hiyo pia inaendana na utekelezaji wa sera ya ushiriki wa Watanzania katika sekta ya madini na inalenga kupunguza utegemezi wa wataalamu kutoka nje ya nchi.

Mitaala hiyo inahusisha mafunzo ya Uendeshaji wa Mitambo ya Kubeba na Kusafirisha Miamba Migodini; Uendeshaji wa Mitambo ya Kuchimba Mahandaki; Uendeshaji wa Mitambo ya Kuchimba Mashimo Marefu, Uendeshaji wa Mitambo ya Kuchimba Mashimo ya Ndani ya Miamba; Maandalizi ya Ulipuaji wa Miamba Chini ya Ardhi,pamoja na Matumizi Salama ya Vifaa vya Kunyanyua na Kufunga Mizigo.

Tarimo amesema mafunzo hayo yatasaidia kujenga nguvu kazi ya Watanzania yenye uwezo wa kushiriki kikamilifu katika shughuli za uchimbaji wa madini na kuchangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.




Na Mwandishi Wetu, Tanga
TAASISI ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo Tanzania (LST) imeondoa matumizi ya karatasi kwa wanafunzi wanaofanya mafunzo kwa vitendo sehemu za kazi (field) katika ofisi na taasisi mbalimbali nchini na kuanza kutumia mfumo wa kidijitali wa kusimamia mafunzo hayo unaotambulika kama LST e-FIELD MIS 2026.

Hatua hiyo inalenga kurahisisha usimamizi wa mafunzo kwa vitendo sehemu za kazi pamoja na kuwawezesha wanafunzi kuwasilisha taarifa zao za mafunzo kwa njia ya kidijitali bila kulazimika kukutana ana kwa ana na wakufunzi wao.

Akizungumza katika maonesho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea jijini Tanga, mkufunzi kutoka LST Bw. Khery Sanga amesema mfumo huo umeondoa vikwazo vilivyokuwa vikimkabili mwanafunzi katika kuwasilisha taarifa zake kwa mkufunzi anayemsimamia.

Amesema kupitia mfumo huo, mwanafunzi huweza kuingiza taarifa za mafunzo yake kila siku moja kwa moja kwenye mfumo, na mkufunzi huweza kuziona na kuzifanyia tathmini.

“Endapo mwanafunzi ataandika taarifa zake katika mfumo na mkufunzi asiridhie, mkufunzi huyo anapaswa kueleza kwenye mfumo sababu ya kutoridhia taarifa hizo” amebainisha.

Aidha ameongeza kuwa mfumo huo unamwezesha mwanafunzi kufanya mawasiliano na kuwasilisha taarifa za mafunzo kwa kutumia simu janja au kompyuta akiwa mahali popote.

Pia mfumo huo unawasaidia wakufunzi kuzipitia kazi wanazofanya wanafunzi wao kila siku wawapo kwenye mafunzo sehemu za kazi.

Sanga amefafanua kuwa LST hutoa mafunzo ya sheria kwa vitendo kwa kipindi cha mwaka mmoja; ambapo katika miezi sita ya kwanza mwanafunzi hujifunza kwa vitendo akiwa darasani, na baada ya hapo huendelea na mafunzo ya vitendo akiwa sehemu za kazi kwa kipindi kingine cha miezi sita.

Sanga ametoa msisitizo kwa wanafunzi wa LST kutumia kikamilifu mfumo huo wa kidijitali ili uweze kuwasaidia kutunza na kuwasilisha taarifa zao kwa ufanisi na hatimaye kuwawezesha kufikia malengo ya mafunzo yao.
Na. Mwandishi wetu, DODOMA


Wizara ya Afya kupitia Idara ya Kinga, Sehemu ya Elimu ya Afya kwa Umma, imewataka wananchi wa Jiji la Dodoma kujitokeza na kuwapeleka watoto wenye umri wa chini ya miaka 10 kupata chanjo ya matone ya Polio, ikiwa ni sehemu ya kampeni ya kuongeza kinga dhidi ya ugonjwa huo.

Akizungumza kuhusu kampeni hiyo, Magdalena Dinawi kutoka Wizara ya Afya, Idara ya Kinga, alisema kuwa chanjo ya Polio inayotolewa kwa njia ya matone ni muhimu katika kuzuia ugonjwa wa kupooza unaosababishwa na virusi vya Polio.

Alisema kuwa ugonjwa huo hauna tiba, hivyo kinga kupitia chanjo ndiyo njia muhimu ya kumkinga mtoto dhidi ya madhara yanayoweza kusababishwa na Polio.

“Chanjo hii ina umuhimu kwa watoto kwa sababu inazuia ugonjwa wa kupooza ambao kitaalamu tunauita Polio. Ugonjwa wa Polio hauna tiba, ila kinga iliyopo ni kwa kupewa matone ya chanjo ya Polio. Aidha, watoto wanatarajiwa kupata huduma hiyo katika vituo vya kutolea huduma za afya, shule, maeneo ya ibada, masoko, magulio na maeneo mengine ambako watoto wenye umri wa chini ya miaka 10 wanapatikana,” alisema Dinawi.

Aliongeza kuwa katika kuhakikisha kampeni hiyo inawafikia watoto wengi, wizara imewashirikisha watu maarufu, viongozi wa dini, wazee wa mila na watu mashuhuri katika Jiji la Dodoma ili kusaidia kuhamasisha jamii kuwapeleka watoto kupata chanjo.

Kwa upande wake, Mratibu wa Huduma za Chanjo wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Victor Kweka alisema kuwa halmashauri hiyo imelenga kuwafikia jumla ya watoto 207,096 wenye umri wa chini ya miaka 10 katika kampeni hiyo.

Aliongeza kuwa halmashauri imeweka mikakati mbalimbali kuhakikisha hakuna mtoto anayekosa chanjo, ikiwemo kutembelea shule zote za awali na msingi pamoja na kufanya kampeni ya nyumba kwa nyumba.

“Tutahakikisha tunapita nyumba kwa nyumba ili kuhakikisha hatuachi mtoto yeyote bila kumpatia chanjo. Tunafahamu kwamba wakati mwingine watoto wanaweza wasiwe shuleni au wasiwe nyumbani,” alisema Kweka.

Aliongeza kuwa timu maalumu zitaelekezwa katika maeneo yenye mkusanyiko wa watu, ikiwemo masoko na vituo vya mabasi, ili kuwafikia watoto ambao huenda wasipatikane shuleni au nyumbani wakati wa utoaji wa chanjo.

Akizungumza katika semina hiyo ya uhamasishaji, mmoja wa viongozi wa dini, Shekh Ahmed Said alishukuru kwa semina hiyo, akiahidi kushirikiana na viongozi wengine wa dini kuhakikisha ujumbe kuhusu umuhimu wa chanjo unawafikia waumini na jamii kwa ujumla.

Wizara ya Afya na Halmashauri ya Jiji la Dodoma zimeendelea kuwahimiza wazazi, walezi na jamii kwa ujumla kutumia fursa hiyo kuwapeleka watoto wenye umri wa chini ya miaka 10 kupata chanjo ya matone ya Polio ili kuongeza kinga kwa watoto, familia, jamii na taifa kwa ujumla.










Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu imeiomba Serikali kuongeza ruzuku kwa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), ili kuwezesha kuongeza kasi ya ujenzi wa nyumba za makazi ya watumishi wa umma nchini.

Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Selemani Kakoso, wakati wa ziara ya kukagua miradi ya nyumba za watumishi inayotekelezwa na TBA katika maeneo ya Kisasa na Nzuguni jijini Dodoma, ikiwa ni sehemu ya ziara ya kutathmini utekelezaji wa miradi ya miundombinu nchini.

Kakoso amesema Kamati imejiridhisha na juhudi zinazofanywa na Serikali pamoja na TBA katika kukabiliana na changamoto ya makazi kwa watumishi wa umma, huku akisisitiza umuhimu wa kuongeza kasi ya ujenzi kutokana na mahitaji makubwa ya nyumba nchini.

Amesema eneo la Nzuguni lenye takribani ekari 630 lililotengwa kwa ajili ya ujenzi wa makazi ni hatua muhimu katika kuendeleza mji mpya wa Serikali, kwa kuwa uwepo wa nyumba hizo utawasaidia watumishi, wakiwemo walio katika ngazi za chini, kupata makazi yaliyo karibu na maeneo yao ya kazi.

“Tunawapongeza Serikali kwa juhudi kubwa zilizofanyika na pia TBA kwa mipango mizuri ya kuandaa nyumba za makazi ya watumishi. Tumekagua eneo la Kisasa na tumeona maboresho makubwa katika nyumba zilizojengwa,” amesema Kakoso.

Hata hivyo, Kamati imeishauri Serikali kuharakisha upatikanaji wa wabia kupitia utaratibu wa Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP), ili kuongeza uwezo wa TBA kutekeleza miradi mikubwa ya nyumba kwa wakati na kukidhi mahitaji ya watumishi.

Kwa mujibu wa Kamati hiyo, ushirikishwaji wa sekta binafsi utawezesha kupatikana kwa mitaji na utaalamu zaidi, huku Serikali ikiendelea kusimamia miradi hiyo kuhakikisha inatoa huduma bora na nyumba zenye viwango vinavyokidhi mahitaji ya watumishi.

Kuhusu huduma ya maji, Kamati imepongeza TBA kwa kuanzisha mfumo wake wa maji bila kutegemea kikamilifu huduma kutoka Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dodoma (DUWASA).

Hata hivyo, imeitaka TBA kuongeza juhudi za kuchimba visima na kuimarisha mifumo ya majitaka ili kukidhi mahitaji ya eneo hilo kwa muda mrefu.

Aidha, Kamati imeishauri TBA kuangalia uwezekano wa kutumia nishati ya jua kama chanzo mbadala cha umeme, hatua ambayo itasaidia kupunguza utegemezi wa mfumo wa kawaida wa umeme na kuhakikisha huduma zinaendelea kupatikana wakati changamoto za umeme zinapotokea.

Vilevile, Kamati imeitaka Wizara ya Ujenzi kushirikiana na Ofisi ya Rais-TAMISEMI, TANROADS, TARURA pamoja na TBA katika ujenzi wa miundombinu bora ya barabara katika maeneo hayo, hususan barabara za lami, ili kuongeza mvuto wa makazi hayo na kurahisisha usafiri.

Kamati imesisitiza kuwa ujenzi wa nyumba za watumishi ni uwekezaji wa muda mrefu unaopaswa kuzingatia thamani ya fedha, ubora wa majengo na mahitaji ya wananchi, ili miundombinu hiyo iwe na tija kwa Serikali na kizazi cha sasa na kijacho.

Naye Mkurugenzi wa Idara ya Miliki wa TBA, Said Rajabu Mndeme, aliyemwakilisha Mtendaji Mkuu wa TBA, amesema mradi huo unatekelezwa katika eneo lenye takribani ekari 640, ambapo ujenzi wa nyumba 150 tayari umekamilika.

Amesema nyumba nyingine 110 zipo katika hatua mbalimbali za ujenzi, zikiwemo nyumba 50 za chini zilizofikia hatua ya mwisho na zinatarajiwa kuanza kutumika. Aidha, majengo mawili ya ghorofa tano yako katika hatua ya msingi, ambapo kila jengo litakuwa na uwezo wa kuhudumia familia 30.

Kwa mujibu wa Mndeme, TBA imeanza kushirikisha sekta binafsi katika utekelezaji wa mradi huo baada ya eneo hilo kutangazwa na wadau mbalimbali wa ndani na nje ya nchi kuwasilisha mapendekezo ya kushirikiana na Wakala.

Amesema mradi huo umepangwa kuwa na huduma muhimu zikiwemo shule za awali, shule mbili za msingi, maeneo ya biashara pamoja na vyuo.

Mndeme amesema mahitaji ya nyumba katika Jiji la Dodoma ni makubwa, akifichua kuwa wakati ujenzi wa nyumba 150 za awali ulipokuwa ukiendelea, TBA ilipokea zaidi ya maombi 1,000 kutoka kwa watumishi waliokuwa wakihitaji makazi.

Amesema hadi sasa, Meneja wa TBA Mkoa wa Dodoma ana maombi zaidi ya 8,000 ya nyumba kutoka kwa watumishi na wananchi, hali inayoonyesha ukubwa wa changamoto ya makazi katika jiji hilo.

Mndeme ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita na Wizara ya Ujenzi kwa kuendelea kuiwezesha TBA kupitia ruzuku, akisema mradi huo ulioanza mwaka 2021 umeendelea kutekelezwa kwa ufadhili wa Serikali.

Amesema TBA sasa inalenga kuongeza kasi ya ushirikishwaji wa sekta binafsi ili kuharakisha ukamilishaji wa mpango wa ujenzi wa nyumba 3,500 na hivyo kupunguza changamoto ya makazi katika Jiji la Dodoma.

Top News