-ASHIRIKI MAADHIMISHO YA MIAKA 10 YA TARI NA SIKU MAALUM YA USHIRIKA
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ameitaka Tume ya Maendeleo ya Ushirika kuendelea kufanya usimamizi wa vyama vya ushirika na kutoa miongozo ya kitaalamu kwa vyama vyote nchini.
Makamu wa Rais ametoa wito huo, wakati wa Siku Maalum ya Ushirika katika Maonesho ya Kimataifa ya Nane Nane kwa mwaka 2026, yanayofanyika katika Viwanja vya John Malecela, Nzuguni mkoani Dodoma.
Amesisitiza Shirika la Ukaguzi na Usimamizi wa Vyama vya Ushirika (COASCO) kuhakikisha linaendelea kufanya ukaguzi wa mara kwa mara kwa vyama vya ushirika kwa lengo la kuhakikisha nidhamu ya matumizi ya fedha, kuzuia ubadhirifu na kuongeza uwazi katika uendeshaji wa vyama hivyo.
Makamu wa Rais, amesema Ushirika wenye uadilifu ni muhimu sana katika kujenga imani kwa wanachama na kuvutia uwekezaji zaidi. Amesema kuimarika kwa ushirika kunategemea uwajibikaji, uaminifu na uadilifu wa wanachama, viongozi na watendaji wa vyama vya ushirika.
Makamu wa Rais ametoa wito kwa taasisi za umma na binafsi, wadau wa maendeleo na wadau wote kuipa ushirikiano Tume ya Maendeleo ya Ushirika katika kufanisha utekelezaji wa Kampeni ya "Linda Ushirika, Chagua Uadilifu" iliyozinduliwa hivi karibuni, inayolenga kutokomeza vitendo vya kihalifu ndani ya Ushirika.
Vilevile, Makamu wa Rais ameielekeza Wizara ya Kilimo kupitia Tume ya Maendeleo ya Ushirika kuhakikisha ushirika unaendana na Dira ya 2050 inayoelekeza Vyama vya Ushirika kuwa na mwelekeo wa kibiashara na kuwa kichocheo muhimu cha ujenzi wa uchumi wa viwanda na ukuaji jumuishi wa Taifa. Pia amesisitiza umuhimu wa kutoa elimu na hamasa zaidi kwa wananchi wote ili kujiunga na vyama vya ushirika na kufikia lengo la Mpango wa Maendeleo wa miaka mitano la kufikisha vyama vya ushirika 20,540,850 ifikapo 2030/2031.
Makamu wa Rais amesema katika kukuza sekta ya kilimo na kuongeza mchango wake katika uchumi wa Taifa, Serikali imedhamiria kutoa huduma bora kwa wakulima zikiwemo pembejeo na huduma za ugani kwa wakati. Mathalan, katika kuongeza matumizi ya mbolea nchini, Serikali inaendelea kuimarisha upatikanaji na kuhimiza matumizi ya mbolea kupitia Mpango wa ruzuku ili kuongeza tija na uzalishaji.
Katika hatua nyingine, Makamu wa Rais ameshiriki Maadhimisho ya Miaka 10 ya Taasisi ya Utafiti wa Kilimo (TARI) yaliyofanyika katika Maonesho ya Nane Nane katika Viwanja vya John Malecela mkoani Dodoma.
Katika maadhimisho hayo, Makamu wa Rais ameipongeza Wizara ya Kilimo, Taasisi ya TARI na wadau wote kwa mchango wao mkubwa katika kipindi cha miaka 10 wa kubuni na kusambaza teknolojia na ubunifu unaoendelea kuleta mageuzi katika sekta ya kilimo na kuboresha Maisha ya wakulima nchini.
Aidha Makamu wa Rais, amewataka watafiti wa Taasisi ya TARI kutafsiri Dira ya Taifa 2050 kuwa matokeo yanayoonekana kupitia tafiti na ubunifu unatoa suluhisho kwa changamoto ya sekta ya kilimo kwa kuongeza tija, ushindani na kuongeza thamani ya mazao.
Amesema historia inafundisha maendeleo ya ukweli na endelevu yanajengwa kwa kuwekeza katika rasilimali watu kupitia elimu bora, sayansi, teknolojia na ubunifu, hivyo Dira ya Taifa 2050 imeweka utafiti na ubunifu kama sehemu ya nguzo muhimu za kujenga uchumi imara na wenye ushindani.
Maonesho ya Kimataifa ya Nane Nane kwa mwaka 2026 yanafanyika katika kauli mbiu isemayo “Tambua soko, ongeza tija, kutekeleza Dira 2050”.
JUBILEE YA MIAKA 100 YA TOSAMAGANGA YAANZA RASMI, BILIONI 1 ZALENGWA KUKAMILISHA MIRADI YA MAENDELEO
MKUU wa Wilaya ya Iringa Benjamin Sitta imezindua rasmi maandalizi ya maadhimisho ya jubilee ya miaka 100 ya Shule ya Sekondari Tosamaganga, huku ikitoa wito kwa wanafunzi wa zamani, wadau wa elimu, taasisi, kampuni na Watanzania wote kushiriki kikamilifu katika kuifanya historia hiyo kuwa ya mafanikio.
Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa uzinduzi huo, Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Benjamini Sitta, alisema shule hiyo iliyoanzishwa mwaka 1926 imekuwa nguzo muhimu ya elimu bora, maadili na uongozi nchini, hivyo maadhimisho ya miaka 100 yanapaswa kuwa fursa ya kuenzi mchango wake kwa taifa.
Alisema maadhimisho hayo yatafanyika chini ya kauli mbiu isemayo, “Miaka 100 ya Elimu Bora, Maadili, na Uongozi wa Kuigwa,” kauli inayobeba historia ya shule hiyo katika kuzalisha viongozi, wataalamu na wazalendo waliolitumikia taifa kwa uadilifu na weledi.
Sitta alisema ratiba ya maadhimisho imeanza kupangwa ambapo Oktoba 8, 2026 kutafanyika matembezi ya Jubilee Walk pamoja na zoezi la usafi wa mazingira kwa lengo la kuhamasisha afya, uzalendo na utunzaji wa mazingira.
Alisema Oktoba 9 kutafanyika mbio za burudani (Fun Run) zitakazowakutanisha wanafunzi wa zamani wa Tosamaganga, wanafunzi wa sasa, wananchi na wadau mbalimbali, huku kilele cha maadhimisho kikitarajiwa kufanyika Oktoba 10, 2026.
Aliongeza kuwa siku ya kilele itahusisha maonyesho ya historia ya shule, nyaraka na kumbukumbu muhimu, vifaa vya kujifunzia na kufundishia, utoaji wa tuzo za heshima pamoja na shughuli mbalimbali zitakazoonesha urithi mkubwa wa taasisi hiyo.
Alisema maadhimisho hayo hayatakuwa ya kusherehekea historia pekee, bali yataacha alama kupitia utekelezaji wa miradi ya maendeleo ikiwemo kuboresha miundombinu ya shule, ununuzi wa basi la wanafunzi na miradi mingine itakayokubaliwa na wadau.
"Huu ni wakati wa wanafunzi wote wa zamani, marafiki wa Tosamaganga na wadau mbalimbali kushiriki kikamilifu na hata waliopo nje ya nchi tunawakaribisha kuungana nasi kuandika historia nyingine ya shule hii ya kipekee," alisema Sitta.
Aliongeza kuwa Serikali ya Mkoa wa Iringa inaamini maadhimisho hayo yatachochea uchumi wa mkoa kutokana na matarajio ya kupokea maelfu ya wageni watakaotumia huduma za malazi, usafiri, chakula, utalii na biashara nyingine mbalimbali.
Sitta alisema Tosamaganga ni shule ya kihistoria yenye usajili namba moja nchini (S1), jambo linaloifanya kuwa sehemu muhimu ya historia ya elimu Tanzania.
Naye Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari Tosamaganga, Laurent Manga, alisema lengo kuu la maadhimisho hayo ni kumshukuru Mungu kwa mafanikio ya shule, kuwakutanisha wanafunzi wa zamani na wadau pamoja na kuhamasisha michango kwa ajili ya kuiboresha taasisi hiyo.
Alisema serikali imekuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya shule hiyo baada ya kutoa zaidi ya shilingi milioni 650 kwa ajili ya ukarabati wa majengo, hatua iliyowezesha wanafunzi kusoma katika mazingira salama na bora zaidi.
Manga alisema kutokana na matokeo mazuri ya kitaaluma, shule hiyo imepewa hadhi ya kuwa shule maalumu (Special School), ambapo sasa inapokea wanafunzi wa kidato cha tano wenye ufaulu wa juu wa alama za pointi 7 hadi 10.
Aidha alisema shule inaendelea kupata huduma muhimu zikiwemo maji, umeme na chakula bila changamoto kubwa, huku akitoa wito kwa wanafunzi wote wa zamani kurejea kushiriki maadhimisho hayo na kuchangia maendeleo ya shule.
"Tunatamani kupata basi la shule ili kuwasaidia wanafunzi katika shughuli mbalimbali za masomo na safari. Hili ni moja ya vipaumbele vyetu katika maadhimisho haya ya miaka 100," alisema Manga.
Kwa upande wake, Mjumbe wa Kamati ya Habari, Hamasa na Matangazo ya maadhimisho hayo, Mwalimu Gayrus Edward Mwakavindi, alisema kamati imeweka lengo la kukusanya shilingi bilioni moja kwa ajili ya kufanikisha maadhimisho pamoja na utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
Alisema michango inaweza kutumwa kupitia akaunti ya CRDB yenye jina la Tosa Maganga Jubilee pamoja na njia nyingine za malipo zilizotengwa kwa ajili ya zoezi hilo.
Mwakavindi alisema kamati ya maandalizi imejumuisha walimu waliowahi kufundisha Tosamaganga, wanafunzi wa zamani wa vipindi mbalimbali, viongozi wa serikali, wanasiasa, wanamichezo na wadau wengine wenye mapenzi na shule hiyo.
Aliwahimiza waandishi wa habari kuendelea kutoa ushirikiano katika kuhamasisha wananchi kushiriki maadhimisho hayo ili kuhakikisha historia ya miaka 100 ya Shule ya Sekondari Tosamaganga inaenziwa na kuacha alama kwa vizazi vijavyo.
📍NIRC: Dodoma
Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC), inaendelea na utekelezaji wa Mkakati mkubwa wa kuimarisha kilimo cha Umwagiliaji
nchini kwa kuzindua miradi mipya zaidi ya 30 katika mwaka wa fedha 2026/27, huku ikitarajia kuajiri maelfu ya vijana kupitia uchimbaji wa visima na usimamizi wa miundombinu ya Umwagiliaji.
Pia inalenga kuongeza uzalishaji wa mazao na kufanikisha azma ya sekta ya kilimo kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.
Akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya Nanenane yanayofanyika katika Viwanja vya Dr. John Malecela, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji Raymond Mndolwa amesema kwa kipindi cha miaka michache ya utekelezaji wa majukumu yake, tume imefanikiwa kuwa na wakandarasi 146 wanaotekeleza miradi mbalimbali ya Umwagiliaji, huku miradi 634 ikiwa katika hatua za usanifu.
Amesema lengo ni kuhakikisha mkulima anakuwa na uwezo wa kuzalisha kwa tija na kuacha kutegemea mvua.
“Tume inatarajia kuanza zoezi kubwa la kugawa pampu za maji katika mikoa saba nchini, ambapo zoezi hili litaanza rasmi mkoani Katavi ifikapo tarehe 11,”amesema
Katika mpango huo, jumla ya pampu za kawaida (surface pumps) 1,000 zitatolewa ili kuwasaidia wakulima wa mbogamboga na matunda kuvuta maji kwa urahisi kutoka kwenye mito na mabonde, jambo ambalo litafanyika kwa njia salama isiyoharibu mazingira.
Sambamba na hilo, zaidi ya pampu 1,000 za kisasa zinazotumia nishati ya jua (solar pumps) zimenunuliwa maalum kwa ajili ya wakulima wa zao la parachichi.
“Wakulima hawa mara nyingi hukumbana na changamoto ya miinuko na mabonde inayokwamisha mifumo ya kawaida ya Umwagiliaji, hivyo pampu hizi ni mkombozi wao mkuu
Ameongeza kuwa “Habari njema zaidi inawaendea vijana mtaani kwani Tume imebuni mradi mkubwa wa uchimbaji wa visima ambao unalenga kuajiri kati ya vijana 2,000 hadi 4,000 ndani ya miaka mitatu ijayo,amesisitiza
Amesema,Mpango huo utahusisha kuunda katika vikundi vijana wenye ujuzi wa ufundi na uhandisi kwenye halmashauri zote 184 nchini.
Aidha Tume itawawezesha vijana hawa kusimamia miradi hiyo na kufunga miundombinu ya visima kwenye maeneo yao badala ya kusubiri waajiriwa kutoka nje.
Mpaka sasa, tayari visima 415 vimechimbwa huku lengo kuu likiwa ni kuchimba visima 67,000 ndani ya miaka nane ijayo.
Akifafanua zaidi kuhusu kazi zinazoendelea, Mkurugenzi Mndolwa amesema Tume imefanikiwa kusimamia mikataba 146 ya ujenzi wa miundombinu ya Umwagiliaji ambapo wakandarasi wapo kazini.
Zaidi ya miradi 634 ipo katika hatua za usanifu na katika mwaka wa fedha 2026/2027, miradi mipya 30 inatarajiwa kuzinduliwa.
KATIKA hatua ya kukuza zao la mkonge nchini na kuongeza ubora wake kwenye masoko ya ndani na nje, Serikali imetangaza mpango wa kununua mashine 10 mpya za kuchakata zao hilo (Dikotiketa/Korona) kwa ajili ya wakulima wadogo.
Sambamba na hilo, Vyama vya Ushirika (AMCOS) vitano wilayani Korogwe, vinatarajiwa kuwekeza kiasi cha Shilingi Bilioni 11.5 kupitia mikopo ya benki kwa ajili ya kusimika mitambo mipya ya kisasa ya kuchakata mkonge.
Lengo la hatua hizo ni kuhakikisha zao hilo linaendelezwa kwa tija, na kuwasaidia wananchi walioamua kulifanya mkonge kuwa zao lao kuu la biashara kupata fursa ya kuvuna na kusindika katika viwango vya ubora wa kimataifa.
Mkakati huo umetangazwa Agosti 2, 2026, na Mkuu wa Sehemu ya Maendeleo ya Mkonge kutoka Bodi ya Mkonge Tanzania (TSB), Bw. Simon Kibasa, wakati akizungumza kwenye Maonesho ya 33 ya Kitaifa ya Kilimo (Nane Nane) yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samwel Malecela, jijini Dodoma.
Usambazaji wa Mashine 10 za Serikali
Kibasa alieleza kuwa, uamuzi wa Serikali kununua mashine hizo 10 umekuja baada ya kubaini kuwepo kwa changamoto kubwa ya vifaa vya uchakataji kufuatia mwitikio mkubwa wa wananchi kuingia kwenye kilimo cha mkonge.
"Kati ya Korona 10 zitakazonunuliwa, tatu zimeshanunuliwa na zimewekwa Taula katika Kata ya Kwedizinga (Handeni), Mbuyuni (Mkinga), na Kijiji cha Komsala (Handeni)," alifafanua Kibasa.
Aliongeza kuwa mashine nyingine zitawekwa Makuyuni, Mswaha, na Mnazi (Korogwe); Miono (Chalinze); Kishapu (Shinyanga); Kilosa (Morogoro); na Daluni (Mkinga). Pia, Serikali kupitia TSB imekarabati mashine kwenye vituo vya Kibaranga wilayani Muheza na Lucy Estate wilayani Arumeru mkoani Arusha.
Uwekezaji Mkubwa wa AMCOS
Akifunua mkakati mzito wa Vyama vya Ushirika, Kibasa alibainisha kuwa AMCOS za mashamba matano wilayani Korogwe (Ngombezi, Magoma, Mwelya, Hale na Magunga), kila moja itanunua Korona mpya kwa kuwezeshwa mikopo na mabenki.
"Kununua Korona moja mpya ni Shilingi Bilioni 1.3, na kuijengea miundombinu ni Shilingi Bilioni 1, hivyo jumla ni Shilingi Bilioni 2.3 kwa kila shamba," alieleza Kibasa, uwekezaji ambao utaleta mapinduzi makubwa ya kiviwanda wilayani humo.
Takwimu za Ukuaji na Mafanikio Chalinze
Akielezea mafanikio ya uhamasishaji uliofanywa na Serikali tangu mwaka 2019/2020, Kibasa alibainisha kuwa idadi ya wakulima wa mkonge nchini imepaa kutoka wakulima 7,551 hadi kufikia takribani 13,000 mwaka 2025/2026.
"Baada ya kuhamasisha, wakulima wengi wameingia. Mfano mzuri ni Wilaya ya Bagamoyo kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Chalinze; hapo mwanzo haikuwa kabisa na wakulima wa mkonge, lakini hadi kufikia Desemba mwaka jana, tulikuwa na wakulima zaidi ya 70 ambao wanamiliki hekta zaidi ya 500," alihitimisha Kibasa, akisisitiza kuwa TSB itaendelea kusimamia ustawi wa zao hilo kikamilifu.
Wadau mbalimbali wametembelea banda la INADES-Formation Tanzania lililopo katika Banda la Mashirika ya Kimataifa na Washirika wa Maendeleo kwenye Maonesho ya Kilimo ya Nanenane yanayoendelea Nzuguni, jijini Dodoma.
Wakati wa ziara hiyo, wadau walipata fursa ya kujifunza mbinu bora za kilimo hai (Agroecology), ufugaji endelevu wa mifugo, pamoja na uhifadhi wa mazingira.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Wanu Hafadh Ameir, amesisitiza nafasi muhimu ya wanawake wanataaluma katika kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Akizungumza jijini Dar es Salaam katika hafla ya Inclusive Mwalimu Gala 2026, Naibu Waziri amesema kuwa kauli mbiu ya hafla hiyo, “The Contribution of Women Professionals to the Implementation of Tanzania Development Vision 2050”, imeakisi mchango wa wanawake katika kujenga uchumi wa maarifa, ubunifu na teknolojia.
Ameeleza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika sekta ya elimu. Hatua zilizotekelezwa ni pamoja na maboresho ya sera na sheria, ujenzi wa miundombinu ya kufundishia na kujifunzia, pamoja na kuimarisha matumizi ya teknolojia katika ufundishaji na ujifunzaji.
Aidha, amesisitiza kuwa mchango wa wanawake hauwezi kupuuzwa na kwamba Serikali ikiendelea kuimarisha usawa wa kijinsia, kuongeza ushiriki wa wanawake katika fani za STEM, kuzuia ukatili wa kijinsia na kuwekeza katika maendeleo ya kitaaluma ya walimu na wahadhiri kupitia mafunzo endelevu na tafiti.
Naibu Waziri ametoa wito kwa walimu, wakufunzi na wahadhiri kuendelea kuwa chachu ya mabadiliko ya Taifa kwa kuandaa kizazi chenye maadili, maarifa na ubunifu.
“Mustakabali wa Taifa upo mikononi mwa vijana na wanafunzi,” amesisitiza, akiwataka kutumia kikamilifu fursa za elimu zinazotolewa na Serikali ili kuleta suluhisho kwa changamoto za kijamii na kiuchumi." amesema Naibu Waziri
Naye Mbunge Viti Maalum Mwakilishi wa Vyuo Vikuu, Mhe. Asha Feruzi, amesema kuwa hafla ya Inclusive Mwalimu Gala 2026 ni jukwaa la kujadili mustakabali wa elimu, ubunifu na teknolojia katika kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Mhe. Feruzi amebainisha kuwa matokeo yanayotarajiwa kupitia ushirikiano huo ni kuimarika kwa tafiti, ubunifu na matumizi ya teknolojia za kisasa, hususan akili unde (Artificial Intelligence). Ameongeza kuwa vyuo vikuu na sekta binafsi vitaunganishwa ili kuzalisha suluhisho, bidhaa na huduma zinazochochea ukuaji wa uchumi shindani na endelevu.






.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)








.jpeg)

.jpeg)



.jpeg)


.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)

