Na Victor Masangu, Bagamoyo

MBUNGE wa Jimbo la Bagamoyo, Mhe. CPA Subira Khamisi Mgalu, ameipongeza Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Bagamoyo kwa ubunifu na mipango madhubuti inayolenga kuongeza ufanisi katika ukusanyaji wa mapato.

Mhe. Mgalu aliyasema hayo wakati wa ziara yake katika Ofisi za TRA Bagamoyo, ambapo alipata fursa ya kukutana na kufanya mazungumzo na Meneja wa TRA Bagamoyo, Mariam Omari.

Katika mazungumzo hayo, walijadili masuala mbalimbali yanayohusu ongezeko la mapato, ukusanyaji wa kodi, mikakati ya kuvuka malengo ya ukusanyaji pamoja na umuhimu wa kuendelea kuwaelimisha na kuwahamasisha wananchi kuhusu ulipaji wa kodi.

Mhe. Mgalu ameipongeza TRA Bagamoyo kwa kazi inayofanyika katika kuhakikisha ukusanyaji wa mapato unaendelea kuimarika, akisema hatua hizo ni muhimu katika kuchochea maendeleo ya Taifa na Jimbo la Bagamoyo.

Aidha, ameahidi kuendelea kutoa ushirikiano kwa TRA na kuhamasisha wananchi kupitia mikutano yake mbalimbali kuhusu umuhimu wa kulipa kodi kwa wakati ili kuwezesha Serikali kutekeleza miradi ya maendeleo.

Mbunge huyo pia amempongeza Meneja wa TRA Bagamoyo, Mariam Omari, kwa moyo wa kujitolea na kushirikiana na jamii, hususan katika kuchangia uboreshaji wa miundombinu katika Shule ya Msingi Ukuni.

Amesema ushiriki wa taasisi na watendaji katika shughuli za kijamii ni mfano mzuri wa ushirikiano kati ya Serikali, taasisi na wananchi, hivyo unapaswa kuungwa mkono na kuendelezwa.

Mhe. Mgalu ameahidi kuwa balozi wa kuhamasisha ushirikiano kati ya wananchi, taasisi na wadau mbalimbali katika kuhakikisha juhudi za maendeleo ya Bagamoyo zinaendelea kuimarika.

Amesisitiza kuwa ushirikiano kati ya viongozi, taasisi na wananchi ni muhimu katika kuongeza uelewa kuhusu ulipaji wa kodi, kuimarisha ukusanyaji wa mapato na kuchochea kasi ya maendeleo.




WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba ameondoka nchini leo (Jumamosi, Septemba 19, 2026) kwenda Roma, Italia kumwakilisha Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Mkutano wa siku tatu wa Kimataifa wa Kujadili Afya Moja na Mifumo ya Chakula na Kilimo. 

Mkutano huo utakaofanyika katika Makao Makuu ya Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), jijini Roma, Italia kuanzia Septemba 21–23, 2026 unalenga kuimarisha utekelezaji wa dhana ya Afya Moja (One Health) inayotambua uhusiano kati ya afya ya binadamu, wanyama, mimea na mazingira, kwa lengo la kuhakikisha mifumo endelevu ya chakula na kilimo

Mkutano huo utahusisha viongozi wa nchi na Serikali, wakiwemo Marais kati ya watano hadi saba, Mawaziri kati ya 30 hadi 50, pamoja na wawakilishi wa taasisi za kikanda na kimataifa, wadau wa maendeleo, sekta binafsi, taasisi za utafiti na mashirika ya kimataifa.

 Mambo muhimu yatakayojadiliwa katika mkutano huo ni Ujumuishaji wa dhana ya Afya Moja (One Health) katika sera na uwekezaji wa mifumo ya chakula na kilimo; na uimarishaji wa ushirikiano wa kisekta kati ya sekta za kilimo, mazingira, afya, fedha na mipango ya miji.

Mengine ni ukuzaji wa ubunifu, sayansi na maarifa ya ndani ili kuboresha uzuiaji wa vihatarishi, ufuatiliaji na usimamizi endelevu wa rasilimali na kuhamasisha uwekezaji na ushirikiano ili kutafsiri ahadi kuwa hatua madhubuti zenye matokeo yanayopimika.





Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius John Ndejembi, amezitaka Taasisi za Muungano kuimarisha ushirikiano, kubaini na kutumia fursa zilizopo pamoja na kushiriki kwa pamoja katika shughuli mbalimbali ndani na nje ya nchi kwa lengo la kuongeza tija na kuleta manufaa zaidi kwa Watanzania.

 Makamu wa Rais ametoa wito huo leo, Septemba 19, 2026 wakati akifungua kikao cha Wakuu wa Taasisi za Muungano kilichofanyika katika Ukumbi wa Golden Tulip, Zanzibar, na kuhudhuriwa na wakuu wa Taasisi 39 za Muungano.

Makamu wa Rais amewataka viongozi wa taasisi hizo kuelewa kwa kina wajibu wao katika kuwahudumia wananchi na kufanya kazi kwa mtazamo mmoja wa kujenga “nyumba moja”, huku maslahi ya Watanzania yakiwekwa mbele.

Amesema matarajio ya wananchi ni kuona Muungano na taasisi zake zikitoa matokeo yanayogusa maisha yao moja kwa moja, hususan katika kuboresha hali ya uchumi, afya, elimu na maeneo mengine muhimu ya kijamii.

 Amezihimiza taasisi hizo kuondoa vikwazo vinavyoweza kudhoofisha ushirikiano na badala yake kutumia fursa zilizopo katika pande zote mbili za Muungano ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao.

Aidha, Mhe. Ndejembi ameahidi kuwa Ofisi ya Makamu wa Rais itaendelea kuunga mkono jitihada za Taasisi za Muungano kwa kuratibu, kusimamia, kushauri na kuziwezesha kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi zaidi, kwa lengo la kuharakisha maendeleo na kuboresha huduma kwa wananchi.

 Akizungumza kabla ya kumkaribisha Makamu wa Rais, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni, amesema kikao hicho kinalenga kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi za Muungano na Ofisi ya Makamu wa Rais; na kuongeza uelewa wa pamoja kuhusu masuala mbalimbali ya Muungano na majukumu yanayotekelezwa na taasisi hizo, sambamba na kuweka mwelekeo wa kuimarisha utendaji kazi na kuongeza ufanisi.

 Kikao hicho cha Wakuu wa Taasisi za Muungano ambacho pia kimehudhiriwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Mhe Hamza Hassan Juma, Makatibu Wakuu na Watendaji Wakuu wa Taasisi kinatoa  nafasi kwa viongozi hao kujadili namna ya kuimarisha uratibu, kubadilishana uzoefu na kuweka mikakati ya pamoja itakayoongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao kwa manufaa ya wananchi






KATIBU wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Itikadi, Uenezi na Mafunzo Taifa, Kenani Kihongosi, amekemea tabia ya baadhi ya wanasiasa kupotosha wananchi kuhusu miradi mikubwa ya maendeleo inayotekelezwa nchini, akisisitiza kuwa CCM haitavumilia upotoshaji wala matumizi ya uongo katika kuwahadaa Watanzania.

Kihongosi aliyasema hayo wakati akizungumza na wananchi wa Wilaya ya Temeke katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Uwanja wa Mafuliza, Toangoma, Dar es Salaam.

Alisema ni muhimu wanasiasa kueleza ukweli kuhusu miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali, badala ya kutumia taarifa zisizo sahihi kwa lengo la kupotosha wananchi.

“Lazima tukubaliane, upotoshaji tutaukemea na anayepotosha hatutamvumilia. Tutamwambia, tusitumie uongo kama silaha ya kudanganya Watanzania, tuwaeleze ukweli,” alisema Kihongosi.

Akizungumzia miradi iliyotekelezwa na Serikali, Kihongosi alisema wakati aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano, Dk. John Magufuli, alipofariki, aliacha miradi mbalimbali mikubwa ikiwa inaendelea kutekelezwa, ikiwemo Reli ya Kisasa (SGR).

Alisema mradi huo umekamilishwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, na sasa wananchi wameanza kutumia huduma ya reli hiyo.

“Wakati Dk. Magufuli anafariki aliacha miradi mingi mikubwa. Mradi wa kwanza ulikuwa Reli ya Kisasa (SGR). Leo ile reli imeisha na wananchi wanatumia. Aliyeikamilisha ni Dk. Samia Suluhu Hassan. Mnyonge mnyongeni, lakini haki yake mpeni. Leo anasimama mtu mmoja na mawazo yake anasema hakuna kilichofanyika,” alisema.

Kihongosi pia alitaja Mradi wa Kituo cha Kuzalisha Umeme cha Julius Nyerere (JNHPP), akisema umekamilika kwa asilimia 100 na tayari umezinduliwa, ukiwa na uwezo wa kuzalisha megawati 2,115 za umeme.

Alisema mradi huo umeongeza uhakika wa upatikanaji wa umeme nchini, huku akitaja pia kukamilika kwa Daraja la Kigongo–Busisi mkoani Mwanza, ambalo sasa linatumika na wananchi.

Kihongosi alisema miradi hiyo ni miongoni mwa ushahidi wa hatua zinazochukuliwa na Serikali katika kuboresha huduma na miundombinu kwa wananchi.












Na Mwandishi Wetu

MKUU wa Wilaya ya Ilala, Edward Jonas Mpogolo, amezindua rasmi Kampeni ya “Safisha Mazingira, Linda Afya” katika Kata ya Kisutu, huku akimpongeza Diwani wa kata hiyo, Tousif Mohammedali Bhojani, kwa kuwa diwani wa kwanza wilayani humo kuanzisha kampeni hiyo.

Mbali na uzinduzi huo, Diwani Bhojani alimkabidhi Mkuu wa Wilaya vifaa mbalimbali vya usafi vilivyotolewa na wadau kwa ajili ya kuunga mkono jitihada za usafi na utekelezaji wa maelekezo ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan pamoja na viongozi wengine, ya kuhakikisha Jiji la Dar es Salaam linakuwa safi.

Uzinduzi huo ulifanyika katika Soko la Baba na Malishe, Kisutu, na kuendelea katika mitaa mbalimbali ya kata hiyo, ukiongozwa na DC Mpogolo akishirikiana na wananchi na wadau wa maendeleo.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mpogolo alimpongeza Diwani Bhojani kwa kuwa diwani wa kwanza katika Jimbo na Wilaya ya Ilala kuzindua kampeni hiyo.

Alisema Wilaya ya Ilala ina jumla ya kata 36 na kwamba Kata ya Kisutu, chini ya uongozi wa Diwani Bhojani, imeonesha dhamira ya dhati ya kutekeleza kwa vitendo kampeni hiyo muhimu ya usafi.

Mpogolo alisema wilaya imeandaa mikakati ya kuzishindanisha kata na mitaa yote ya maeneo ya katikati ya jiji (CBD) katika suala la usafi, huku kata na mitaa itakayofanya vizuri ikitarajiwa kupewa zawadi.

“Katika kuhamasisha suala la usafi, tumeandaa zawadi ambazo zitatolewa kwa kata na mitaa ya mjini, yaani CBD, itakayofanya vizuri katika usafi. Lengo ni kuhamasisha kampeni hii ya usafi katika wilaya yetu. Kisutu mmeonesha mfano kwa kuwa kata ya kwanza kuzindua kampeni hii muhimu,” alisema Mpogolo.

Aidha, alisema Wilaya ya Ilala itaendelea kutekeleza kwa vitendo maelekezo ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, kwa kuhakikisha usafi unakuwa sehemu ya utamaduni wa wananchi, kuanzia ngazi ya mtu mmoja, familia hadi jamii nzima.

“Tunaenda kutekeleza sheria zetu ndogo kwa wananchi watakaokiuka sheria za usafi. Wale watakaovunja sheria tutawakamata na kuwafikisha katika Mahakama ya Jiji. Akipatikana na hatia atalipishwa faini au kifungo,” alisema.

Aliwataka wananchi wa Kata ya Kisutu na Wilaya ya Ilala kwa ujumla kuhakikisha wanazingatia kanuni za usafi, ikiwemo kuwa na vifaa vya kuhifadhia taka na kufuata sheria na taratibu zinazohusu usafi wa mazingira.

Kwa upande wake, Diwani Bhojani alisema kata hiyo imejipanga kikamilifu kuhakikisha inadumisha usafi, ikieleza kuwa usafi hautakuwa shughuli ya Jumamosi pekee au wakati wa kampeni, bali utakuwa sehemu ya maisha ya kila siku.

“Hivi karibuni Rais Dk. Samia alitamka kuwa Jiji ni chafu. Tamko lile lilikuwa ni ujumbe kwetu. Tuko tayari kutekeleza kwa vitendo agizo hilo,” alisema.

Alisema tangu Rais alipotoa kauli hiyo, Kata ya Kisutu imeendelea kufanya usafi na kuwataka wadau mbalimbali kuendelea kujitokeza kushiriki katika kampeni hiyo.






Na Mwandishi Wetu, Nzega

MWENGE wa Uhuru umezindua mradi wa upanuzi wa mfumo wa kusafisha na kutibu maji unaotekelezwa na Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Nzega Mjini (NUWASA), huku ukielezwa kuwa utasaidia kuimarisha upatikanaji wa maji kwa wananchi.

Mradi huo umezinduliwa leo, Septemba 19, 2026, na Mkuu wa Wilaya ya Nzega, Mhe. Naitapwaki Tukai, mbele ya Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa kwa mwaka 2026, Wazo Michael Mwang'onda.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mhe. Tukai amesema kukamilika kwa mradi huo kutasaidia kuimarisha upatikanaji wa maji safi na salama, sambamba na kupunguza magonjwa ya mlipuko yanayoweza kusababishwa na ukosefu wa maji.

Amesema mradi huo pia umewawezesha wananchi wa Mji wa Nzega kupata huduma ya maji kulingana na mahitaji na uwezo wao wa kulipia.

“Wananchi wa Mji wa Nzega wanatumia maji kadiri wanavyohitaji kupitia mradi huu. Wananchi wanaweza kulipia kiasi wanachohitaji; wakitaka maji ya Shilingi 3,000 wanapata na wakitaka ya Shilingi 100,000 pia wanapata,” amesema.

Kwa upande wake, Meneja wa Mradi huo, Mhandisi Salum Yasin Ikinda, amesema mradi umetekelezwa kwa kipindi cha miezi 36 na umejengwa na kampuni ya FABEC Investment Ltd.

Amesema mradi huo umetekelezwa kwa gharama ya Shilingi 620,103,998.30, ambapo hadi sasa mkandarasi ameshalipwa Shilingi 290 milioni.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2026, Wazo Michael Mwang'onda, ameipongeza Nzega kwa utekelezaji na ubora wa mradi huo.

“Kutokana na ubora wa mradi huu, hapa panapaswa kulindwa kwa wivu mkubwa ili kuhakikisha unakuwa endelevu kwa maslahi mapana ya jamii ya eneo hili,” amesema Mwang'onda.




Na Mwandishi wetu, Nzega 

MWENGE wa uhuru umezindua mradi wa Nkuba hotel (Pride of Nzega) iliyopo mjini Nzega Mkoani Tabora wenye thamani ya shilingi 274,000,000.

Mkuu wa Wilaya ya Nzega Mhe Naitapwaki Tukai akizungumza mbele ya kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru kitaifa mwaka 2026 Wazo Michael Mwang'onda amesema wanampongeza mmiliki wa hoteli hiyo Ndongo Mabula kwa uwekezaji huo.

Amesema mradi huo ni ishara ya sekta binafsi kuunga mkono juhudi za Serikali kukuza uchumi, kuvutia wageni, kuongeza matumizi yenye tija ya ardhi na kutoa ajira kwa wananchi.

"Mradi huu utaboresha mazingira ya upatikanaji wa huduma za hoteli na ukumbi wa kisasa wa mji wa Nzega, wageni watapata sehemu ya kupumzika na halmashauri ya mji itapata kodi," amesema DC Tukai.

Edina Eliberatus akisoma taarifa ya ujenzi kwa niaba ya mmiliki wa hoteli hiyo Ndongo Mabula amesema ujenzi wa mradi ulianza rasmi Machi mosi mwaka 2025 na kukamilika Septemba 4 mwaka 2026.

Amesema gharama za mradi huo wa hoteli ni shilingi 24,000,000 unahusisha vyumba 12 vya kulala wageni na ukumbi mmoja wa mikutano.

"Tunaishukuru Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe Rais DKt Samia Suluhu Hassan kwa kuweka mazingira bora ya uwekezaji kwa sekta binafsi," amesema Mabula.

Kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru kitaifa mwaka 2026 Wazo Michael Mwang'onda amempongeza mwekezaji wa hoteli hiyo Ndongo Mabula kwa ujenzi wa mradi huo.

Mwang'onda amesema mwekezaji amejenga bila kuwekewa mikwamo hivyo Serikali ya Wilaya ya Nzega inastahili pongezi kubwa.

"Mwekezaji anapotaka kuwekeza mradi asiwekewe mikwamo na vikwazo wapeni kipaumbele kwani hata Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan amekuwa akisisitiza sekta binafsi kupewa kipaumbele hivyo Nzega hongereni sana," amesema




Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

KATIBU wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Kenani Kihongosi, amesema miradi inayotekelezwa kwa fedha za umma inapaswa kwenda kwa kasi na kuzingatia ubora unaostahili ili wananchi wanufaike na uwekezaji unaofanywa na Serikali.

Kihongosi ametoa kauli hiyo leo, Septemba 19, 2026, baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa Barabara za Masuliza na Kilimahewa–Tuangoma katika Wilaya ya Temeke, Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya siku mbili katika Mkoa wa Dar es Salaam.

Amesema hajaridhishwa na kasi ya utekelezaji wa ujenzi wa barabara hizo na kusisitiza kuwa mkandarasi anayeshindwa kutekeleza kazi kwa kiwango kinachokubalika anapaswa kuchukuliwa hatua.

“Kama mkandarasi analeta mambo yasiyofaa, achukuliwe hatua na aelezwe kwamba Chama hakijaridhishwa na namna anavyofanya kazi zake katika kutengeneza hii miradi,” amesema Kihongosi.

Amesema CCM na Serikali hazitaruhusu uzembe katika utekelezaji wa miradi inayogharamiwa na fedha za umma, kwa kuwa wananchi wanatarajia kuona matokeo yenye tija kwao na kwa Taifa kwa ujumla.

Kihongosi amesisitiza kuwa msimamo huo unaendana na maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuhakikisha miradi ya maendeleo, hususan miundombinu, inatekelezwa kwa kuzingatia viwango vya ubora na kwa wakati.

Barabara hizo zinajengwa chini ya Mradi wa Uendelezaji wa Jiji la Dar es Salaam Awamu ya Pili (DMDP II), ambapo Barabara ya Masuliza ina urefu wa kilomita 4.04, huku Kilimahewa–Tuangoma ikiwa na urefu wa kilomita 7.3.

Ujenzi wa barabara hizo unatekelezwa na GroupSix International Ltd kwa gharama ya Sh bilioni 25.99.

Kwa mujibu wa taarifa ya DMDP II, Wilaya ya Temeke imepangiwa kutekeleza ujenzi wa barabara 42 zenye jumla ya urefu wa kilomita 55.449, zilizogawanywa katika mafungu saba na kusimamiwa na wakandarasi mbalimbali.

Mikataba ya mafungu manne ya kwanza, yenye jumla ya kilomita 32.8, ina thamani ya Sh bilioni 97.17 na utekelezaji wake unaendelea, wakati mafungu matatu yaliyosalia yako katika hatua ya usanifu.

Kupitia DMDP II, Serikali inalenga kuboresha miundombinu ya barabara pamoja na huduma nyingine muhimu katika Manispaa ya Temeke, kwa lengo la kuboresha mazingira ya maisha na shughuli za kiuchumi kwa wananchi.









Na Mwandishi Wetu
SHINDANO la kumsaka mrembo wa Kanda ya Mashariki 'Miss Eastern Zone' limezinduliwa kwa kishindo jana usiku Wilayani Mkuranga Mkoa wa Pwani.

Akizindua shindano hilo Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga Khadija Nassir amesema kuwa urembo mashindano ya 'Miss Tanzania'

Kanda ya Mashariki 2026 yana nafasi ya kuwa jukwaa la kukuza vipaji vya wasichana na kuwafungulia fursa za ajira.

Amesema hayo alipokuwa mgeni rasmi kwenye uzinduzi huo uliofanyika Kisemvule Mkoani Pwani pia amewataka wadau na wawekezaji kujitokeza na kutoa udhamini.

DC Khadija amesemakuwa kuwa Serikali kwa kupitia Wilaya hiyo itaendelea kushirikiana na waandaaji kuhakikisha mashindano yanafanyika kwa ufanisi.

Amesema uzinduzi huo ni tukio la kihistoria kwa Mkuranga pamoja na kutoa fursa ya kuitangaza Wilaya hiyo pamoja na fursa zake kwa watu kutoka ndani na nje ya eneo hilo.

“ Uzinduzi huu uliofanyika leo tarehe 18 Septemba 2026 Mkuranga umeandika historia kwa kuweza kuasisi jambo hili kubwa, ambalo linaenda sambamba na sera ya Serikali katika kuhakikisha tunaendelea kukuza sanaa na kuweka mazingira wezeshi kwa sanaa za aina zote kuibua ajira mbalimbali kwa vijana wetu,” amesema.

DC Khadija amewataka wawekezaji na kampuni mbalimbali kujitokeza kudhamini mashindano hayo, amesema ushiriki wa sekta binafsi utasaidia kuongeza ukubwa na mafanikio.

Kwa upande wake, Yusuf Hassan, Mkurugenzi wa Miss Tanzania Kanda ya Mashariki, amesema mshindi atazawadiwa gari, huku washindi wa nafasi nyingine wakipata zawadi pamoja na fursa za kuwa mabalozi wa Kampuni na taasisi zitakazoshirikiana na mashindano hayo.

Amesema zawadi hiyo ya gari imetokana na ushirikiano wa wadau mbalimbali, akiwamo DSTV, Fursa Hub, Kairuki Hospital, Lamata Village na Lamata Foundation.

Aidha, amesema bado wanahitaji wadhamini wakubwa zaidi kwa kuwa bajeti ya mashindano hayo inakadiriwa kufikia takribani Sh Mil. 210, hivyo kuwataka wadau kuendelea kujitokeza.

Yusuf amesema mashindano hayo yatahusisha Mikoa ya Morogoro, Lindi, Mtwara na Pwani, huku warembo 16 watakaofaulu usaili wakitarajiwa kuingia kambini kuanzia Oktoba Mosi kwa ajili ya mafunzo mbalimbali.

Amesema mafunzo hayo yatajikita katika urembo, masuala ya kijamii, uongozi, uchumi na fedha, kabla ya fainali iliyopangwa kufanyika Oktoba 10, 2026.

Miss Tanzania 2022 Halima Kopwe, aliyetokea Kanda ya Mashariki 2022 amesema mashindano ya urembo yamekuwa sehemu muhimu ya safari yake na yalimfungulia fursa mbalimbali baada ya kushiriki shindano la kanda hiyo na baadaye kushinda taji la Miss Tanzania.

Halima, ambaye aliiwakilisha Tanzania katika mashindano ya 'Miss World,', amesema kabla ya kuwa Miss Tanzania alikuwa Miss Mtwara na baadaye kuingia kwenye Kanda ya Mashariki iliyomsaidia kufikia mashindano ya kitaifa.

Naye Hidan Ricco, mwakilishi wa Kamati ya Miss Tanzania iliyo chini ya Lamata Village Entertainment Company Limited, amesema wanafurahishwa kuona mashindano ya kanda yakianza baada ya kuzinduliwa kwa Miss Tanzania wiki iliyopita.

Ricco amesema Kanda hiyo imekuwa kanda ya kwanza kuzindua mashindano yake baada ya uzinduzi wa mashindano ya kitaifa, akisema hatua hiyo inaonesha mwendelezo wa mchakato wa Miss Tanzania.


 MKURUGENZI wa Shule ya Green Acres ya Mbezi Beach Salasala, jijini Dar es Salaam, Jackline Rushaigo, amesema shule hiyo imeanza kufundisha Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), ikiwemo akili mnemba, ili kwenda sanjari na ulimwengu wa kidijitali.

Akizungumza kwenye mahafali ya Darasa la Saba na shule ya awali, ambapo wanafunzi 60 walihitimu elimu ya msingi, Rushaigo alisema shule hiyo inatambua umuhimu wa kuzingatia teknolojia za kisasa katika ufundishaji.

 “Tumeongeza ubora na ufanisi kwenye TEHAMA, wanafunzi wetu wanajifunza masuala ya akili mnemba wakiwa wadogo hapa shuleni na mambo yanayoendana na uhalisia wa Utanzania wetu na dunia ya sasa,” alisema.

“Tunawapa taaluma ambayo hata wakiwa nje ya shule wanaweza kufanya vitu mbalimbali vya kujiajiri na kujiingizia kipato. Green Acres tunataka mwanafunzi akimaliza hapa awe na ujuzi wa kutosha kabisa kumwezesha kufanya mambo makubwa,” alisema.

Aliwataka wahitimu wa Darasa la Saba kuendelea kuwa na nidhamu, bidii na kujituma katika masomo wanapoingia katika hatua nyingine ya elimu, huku akisema mafanikio ya mwanafunzi hayawezi kutenganishwa na ushirikiano wa karibu kati ya shule, walimu, wazazi na walezi.

Rushaigo aliwashukuru wazazi na walezi kwa kuiamini Green Acres na kushirikiana na uongozi wa shule katika kuwalea na kuwaandaa watoto wao kwa maisha ya baadaye. Alisema Green Acres itaendelea kuwekeza katika elimu inayolenga kumjenga mwanafunzi kitaaluma, kimalezi na katika nyanja mbalimbali za maisha.

Mgeni rasmi katika mahafali hayo, Edwin Odemba, aliwataka wahitimu kuendelea kuthamini elimu, nidhamu na maadili mema wanapoingia katika hatua nyingine ya masomo yao.

 Aliwapongeza kwa kumaliza elimu ya msingi na kuwataka kutumia maarifa waliyoyapata shuleni kama msingi wa kujenga maisha yao ya baadaye.

Odemba aliwataka wazazi kuendelea kushirikiana na walimu katika malezi na elimu ya watoto, akieleza kuwa mafanikio ya mwanafunzi yanahitaji ushirikiano wa familia, shule na jamii kwa ujumla. Pia aliwapongeza walimu na uongozi wa Green Acres kwa mchango wao katika kuwaandaa wanafunzi kitaaluma na kimalezi.

Aliwataka wahitimu kutambua kuwa kumaliza Darasa la Saba si mwisho wa safari yao, bali ni mwanzo wa hatua nyingine muhimu inayohitaji kujituma, kujiamini na kuweka malengo ya muda mrefu, huku akiwahimiza kuwa mabalozi wema wa shule yao na kutumia elimu yao kwa manufaa yao, familia zao na jamii.







Top News