Msanii na mtayarishaji wa filamu nchini na Diwani wa Viti Maalum Wilaya ya Kinondoni, Councillor Lilian Shirima "Manka amesema amewahi kukutana na changamoto ya kushinikizwa kufanya ngono ili apewe nafasi za kuigiza, akieleza kuwa hali hiyo iliwahi kuwa miongoni mwa vikwazo vilivyowakabili waigizaji wanawake katika safari ya kutafuta ajira kwenye sekta ya sanaa.
Hayo ameyasema wakati wa uzinduzi wa Tamthiliya yake mpya iitwayo “Mbalamwezi” inayorushwa kwenye king’amuzi cha Azam ambaoi amesema waigizaji wanafanya kazi ili kujipatia kipato na kusaidia familia zao, hivyo haikuwa sahihi kutumia nafasi za kazi kama njia ya kuwanyonya.
Amesema changamoto hiyo ilimkuta mara kadhaa, ambapo baada ya kufanya casting na kuonesha uwezo wake, baadhi ya watu waliokuwa na mamlaka ya kutoa nafasi walimuita katika mazingira binafsi na kuanza kutoa masharti yasiyohusiana na kazi.
“Unakuta unaenda, unapewa casting, unatoa scene tatu au nne, lakini mwisho wa siku producer anakuita na kuanza kukwambia mambo mengine. Sasa ni wewe kukubali au kukataa. Ukikataa, huyo mtu anakasirika na casting zako zinachukuliwa na kupewa mtu mwingine,” amesema.
Hata hivyo, amesema hali ya sasa inaweza kuwa tofauti kutokana na kukua kwa soko la sanaa, kuongezeka kwa maproducer na kuwepo kwa fursa nyingi zaidi kwa wasanii.
Amesema changamoto hizo zilimjengea nguvu ya kufanya kazi kwa bidii na kumuomba Mungu ili kufanikiwa bila kutegemea mtu mmoja.
“Ilinipa focus sana kufanya kazi kwa bidii ili na mimi niweze kufanya kazi yangu. Ilinishawishi niwe mwombaji sana, nikamwomba Mungu sana, ili ule mtu ajue kwamba bila yeye pia kuna Mungu,” amesema.
Akizungumzia uzoefu wake wa kufanya kazi na Azam, amesema si rahisi kupata nafasi ya kuingiza kazi katika kituo hicho, bali kinachoweza kumsaidia mtayarishaji ni kuwa na kazi yenye ubora, maudhui ya Kitanzania na Afrika pamoja na kuzingatia maadili.
Amesema kazi hupitia mchakato mkali wa uchambuzi wa maudhui kabla ya kuidhinishwa, huku script, uzalishaji, lugha, mavazi na masuala mengine yakizingatiwa. “Azam wanataka story yenye maudhui ya Afrika, maudhui ya Tanzania. Wanazingatia maadili, kuanzia maneno, matamshi, mavazi na muonekano wa mtu,” amesema.
Aidha, amewashauri watayarishaji chipukizi kutokata tamaa, bali kujenga kampuni zilizosajiliwa na kufuata taratibu za kisheria, huku wakihakikisha wana timu yenye weledi na vifaa vyenye ubora. Amesema mafanikio katika sekta hiyo yanahitaji maandalizi, ubunifu na uzalishaji bora. “Unaweza ukaproduce kazi nzuri lakini ukakosa mtu wa kukushika mkono. Kwanza lazima uwe na kampuni, uisajili BRELA na kufuata taratibu zinazohitajika. Lakini pia production yako iwe imesimama na crew yako iwe na watu wanaojua wanachotakiwa kufanya,” amesema.



.jpeg)

.jpeg)








.jpeg)



.jpeg)

.jpeg)





















.jpeg)



.jpeg)




