Na Janeth Raphael - MichuziTv - Bungeni Dodoma.
Serikali imesema imeweka mikakati mbalimbali ya kukuza vipaji na ujuzi kwa vijana wenye ulemavu, kuwawezesha kupata ajira zenye staha na kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi.
Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Dkt. Jafar Seif, wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Yumna Mmanga Omar, lililohusu mkakati mahsusi wa Serikali wa kukuza vipaji na ujuzi kwa vijana wenye ulemavu ili kuongeza ajira na ushiriki wao katika uchumi.
Akijibu swali hilo, Dkt. Seif amesema Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2025–2030, hususan Kifungu cha 95, imeweka msisitizo wa kuwashirikisha na kuwawezesha watu wenye ulemavu kupata ajira zenye staha pamoja na kujenga uwezo wao ili washiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi.
Amesema Serikali pia inatekeleza Mkakati wa Kitaifa wa Kukuza na Kuendeleza Vipaji na Ujuzi kwa Vijana unaoongozwa na Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Vijana ya mwaka 2007, Toleo la mwaka 2024.
Kwa mujibu wa Dkt. Seif, Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 nayo imeweka mkazo katika kukuza elimu jumuishi na kuhakikisha vijana wenye ulemavu wanapata fursa sawa katika elimu, mafunzo ya ufundi, ajira na shughuli mbalimbali za kiuchumi.
Amesema mikakati hiyo inalenga kuhakikisha ulemavu hauwi kikwazo kwa mtu kutumia kipaji, uwezo na ujuzi wake katika kujenga maisha yake na kuchangia maendeleo ya Taifa.
Katika utekelezaji wa mikakati hiyo, Serikali imewezesha vijana wenye ulemavu kupata mafunzo ya ufundi stadi katika maeneo mbalimbali nchini.
Dkt. Seif amesema jumla ya vijana 643 wenye ulemavu walijiunga na kuhitimu mafunzo ya ufundi stadi katika vyuo vitano, vikiwemo vya VETA, katika kipindi cha mwaka 2023 hadi 2025.
Amesema vijana hao walipata ujuzi katika fani mbalimbali zikiwemo umeme wa majumbani, useremala, uungaji vyuma, ushonaji wa nguo na viatu, kilimo na ufugaji, pamoja na ujenzi na uashi.
Mbali na mafunzo, Serikali imeendelea kuweka mazingira ya kuwawezesha vijana wenye ulemavu kutumia ujuzi walioupata katika kujiajiri na kushiriki katika uchumi.
Dkt. Seif amesema Serikali imetenga asilimia 30 ya zabuni za umma kwa ajili ya kuwawezesha makundi yanayolengwa, ambapo hadi mwaka 2024/25 jumla ya vikundi 703 vya watu wenye ulemavu vilikuwa vimesajiliwa katika mfumo wa NeST.
Hatua hiyo inalenga kuhakikisha kuwa ujuzi na vipaji vinavyopatikana kupitia mafunzo vinaweza kugeuzwa kuwa fursa za ajira, ujasiriamali na kujikwamua kiuchumi.
Aidha, Serikali imeendelea kutenga asilimia 10 ya mapato ya Halmashauri kwa ajili ya mikopo kwa makundi maalum, ambapo asilimia mbili hutengwa kwa ajili ya watu wenye ulemavu.
Katika kipindi cha mwaka 2021 hadi 2026, Serikali imesema jumla ya Shilingi bilioni 26.87 zimetolewa kwa ajili ya kuwawezesha watu wenye ulemavu kupitia mikopo hiyo.
Serikali imesisitiza kuwa hatua hizo ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha vijana wenye ulemavu wanapata fursa sawa za kujenga vipaji, kupata ujuzi, kuajiriwa au kujiajiri na hatimaye kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii ya Taifa.