Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki (Mb), amesema Tanzania inaendelea kuweka mazingira wezeshi ili wananchi wote wapate huduma za mawasiliano zilizo jumuishi, nafuu, salama na zenye uhakika, sambamba na kuimarisha ujuzi wa kidijitali na matumizi yenye tija ya teknolojia.

Waziri Kairuki ameyasema hayo wakati akishiriki Mkutano wa Saba wa Jukwaa la Sera za Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (WTPF-26), unaofanyika Nassau, Bahamas, ambapo amesema hatua hizo zinalenga kutekeleza Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 na Mkakati wa Taifa wa Uchumi wa Kidijitali 2024–2034.

Amesema Tanzania imekamilisha ujenzi wa minara 758 ya teknolojia ya 4G, hatua iliyowezesha zaidi ya vijiji 1,400 na takribani wananchi milioni 8.5 waliokuwa hawapati huduma za mawasiliano ya uhakika kuunganishwa na huduma hizo.

Aidha, kupitia Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Serikali imeanzisha Vilabu vya Kidijitali 800 kwa ajili ya kujenga ujuzi wa TEHAMA, kuwezesha huduma za Wi-Fi katika maeneo 100 ya umma na kujenga maabara za kompyuta katika shule 250 za umma, zikiwemo huduma zinazozingatia mahitaji ya wanafunzi wenye ulemavu.

Akieleza vipaumbele vya Tanzania katika kuziba pengo la kidijitali, Waziri Kairuki amesema nchi inalenga kupanua huduma za mawasiliano kwa gharama nafuu, kuongeza ujuzi wa kidijitali na matumizi ya Akili Unde (AI), pamoja na kuendeleza miundombinu ya kidijitali iliyo salama, jumuishi na inayolinda taarifa binafsi za watumiaji.

Waziri Kairuki amesema Tanzania iko tayari kushirikiana na Umoja wa Kimataifa wa Mawasiliano (ITU) na wadau wengine wa maendeleo kuimarisha ujuzi wa kidijitali na matumizi ya Akili Unde barani Afrika. Amesisitiza kuwa mafanikio ya mageuzi ya kidijitali hayapaswi kupimwa kwa idadi ya minara pekee, bali kwa namna teknolojia inavyoboresha maisha, kuongeza fursa za kiuchumi na kijamii na kuhakikisha hakuna anayebaki nyuma katika uchumi wa kidijitali.


 


KAMPUNI ya Uchimbaji Madini ya Barrick imeeleza kuridhishwa na huduma za kodi zinazotolewa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na kusifu mazingira ya kodi ambayo ni shirikishi kwa wananchi.

Kauli hiyo imetolewa na Meneja Mkazi wa Barrick Gold Mine Tanzania  Melkiory Ngido wakati wa kikao baina ya Uongozi wa Kampuni hiyo na Kamishna Mkuu wa TRA Yusuph Juma Mwenda katika ofisi za TRA jijini Dar es Salaam. 

Ngido amesema utaratibu uliowekwa na TRA wa kufungua milango na kukutana na Walipakodi kujadili masuala mbalimbali ya kikodi umekuwa na tija katika kuongeza uelewa wa kodi na kuhamasisha ulipaji wa kodi kwa hiari. 

"Sisi tumekuwa na utaratibu wa kila mwaka kukutana na Uongozi wa TRA kueleza hali yetu ya kibiashara na namna tutakavyolipa kodi, na kama ambavyo imekuwa kwa vipindi vingine hali yetu kibiashara ni nzuri na tutaendelea kulipa kodi kwa hiari" amesema Ngido. 

Kwa upande wake Kamishna Mkuu wa TRA Yusuph Juma Mwenda amesema Mamlaka hiyo itaendelea kuboresha huduma zake kwa walipakodi, kutoa elimu ya kodi na kuwezesha biashara. 

Amesema TRA inatambua na kuthamini mchango wa Kodi wa Barrick Gold Mine wakiwa ni walipakodi wakubwa pamoja na walipakodi wengine kote nchini na kuwa milango ya taasisi hiyo ya Umma ipo wazi kwaajili ya kuwasikiliza na kutatua changamoto zinazowakabili walipakodi kote nchini.




Na Janeth Raphael - MichuziTv Bungeni Dodoma 

Mafunzo kwa vijana yanatarajiwa kwenda zaidi ya kuwapatia ujuzi, huku msisitizo ukiwekwa katika kuwaunganisha na ajira, mitaji, masoko na fursa za uzalishaji ili waweze kujiajiri na kuanzisha biashara endelevu.

Hayo yameelezwa Bungeni na Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Zainab Katimba, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana, wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Zulfa Mmaka Omary, aliyetaka kujua namna Serikali inavyohakikisha programu za mafunzo na uwezeshaji kwa vijana zinazalisha ajira halisi na endelevu.

Zulfa alihoji kuhusu mkakati mahsusi wa kuhakikisha ajira na uwezeshaji wa vijana haviishii katika kuwapatia mafunzo pekee, bali vinawasaidia vijana kupata ajira, kujiajiri na kuwa na shughuli za kiuchumi zenye uwezo wa kudumu.

Akijibu, Naibu Waziri Katimba amesema mafunzo yanayotolewa kwa vijana yanaelekezwa zaidi katika mahitaji ya soko la ajira na fursa zilizopo katika shughuli za uzalishaji.

Amesema hatua hiyo inaambatana na mafunzo kwa vitendo, uanagenzi na kuwapatia vijana uzoefu wa kazi, sambamba na kuwaunganisha na mitaji, vifaa na zana za uzalishaji.

 Katimba, amesema mkakati huo unatekelezwa kupitia programu mbalimbali za uwezeshaji vijana, zikiwemo Programu ya Kukuza Ujuzi, Build for Better Tomorrow, Mining for a Brighter Tomorrow, pamoja na Programu ya Uwezeshaji Vijana Kiuchumi yenye Shilingi bilioni 200.

Programu nyingine ni Mfuko wa Maendeleo ya Vijana, mikopo ya asilimia 10 ya mapato ya ndani ya Halmashauri, pamoja na programu zinazotekelezwa na SIDO na VETA.

Aidha, amesema vijana wanaunganishwa na waajiri, taasisi za fedha, wawekezaji, masoko pamoja na fursa za ununuzi wa umma ili kuwawezesha kutumia ujuzi walioupata katika kupata ajira au kuanzisha na kukuza biashara zao.

Amesema uwezeshaji huo unaenda sambamba na ushauri wa kitaalamu, uatamiaji wa biashara, uunganishaji wa vijana katika minyororo ya thamani na masoko, pamoja na ufuatiliaji wa miradi wanayoianzisha.

Hatua hizo, kwa mujibu wa Naibu Waziri, zinalenga kuhakikisha vijana wanapata mazingira yanayowawezesha kutumia ujuzi wao kuzalisha kipato, kujenga biashara zinazodumu na hatimaye kutoa ajira kwa vijana wengine.

Amesema utekelezaji wa mikakati hiyo unafanyika kwa kushirikiana na sekta binafsi pamoja na wadau wengine wa maendeleo, kwa lengo la kujenga mfumo unaomsaidia kijana kuanzia hatua ya kupata mafunzo hadi kufikia ajira, kujiajiri au kukuza biashara yenye tija.








Na Janeth Raphael - MichuziTv Bungeni Dodoma


SERIKALI imesema itaendelea kuboresha utoaji wa mikopo ya asilimia 10 kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kwa kuimarisha matumizi ya wataalamu wa mafunzo ya biashara, hatua inayolenga kuongeza ufanisi na manufaa ya mikopo hiyo kwa wajasiriamali nchini.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), anayeshughulikia Elimu, Dkt. Festo Dungange, wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Chiku Athman Issa.

Katika swali lake, Mbunge Chiku alitaka kujua iwapo Serikali inaona kuwa sababu kubwa ya mikopo ya asilimia 10 kutokuwa na matokeo makubwa tangu kuanza kwake ni ukosefu wa wataalamu wa kutoa mafunzo ya biashara kwa wanufaika.

Akijibu, Dkt. Dungange amesema Serikali inaendelea kutoa mikopo hiyo kwa mujibu wa Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa, Sura ya 290, pamoja na Kanuni zake za mwaka 2024, ambazo zinaweka utaratibu wa ukopaji, urejeshaji na usimamizi wa mikopo hiyo.

Amesema lengo la mikopo hiyo ni kuwawezesha wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kupata mitaji midogo na ya kati isiyo na riba kupitia mapato ya ndani ya halmashauri, ili kuwawezesha kuendesha shughuli za ujasiriamali na kurejesha mikopo kwa ajili ya kuwanufaisha wajasiriamali wengine.

Dkt. Dungange amesema katika kipindi cha mwaka wa fedha 2024/25 hadi 2025/26, jumla ya vikundi 33,594 vya wajasiriamali vilinufaika na mikopo hiyo.

Amefafanua kuwa kati ya vikundi hivyo, 18,539 vilikuwa vya wanawake, 11,758 vya vijana na 3,247 vya watu wenye ulemavu, huku jumla ya Sh bilioni 357.20 zikitolewa kwa vikundi hivyo.

Dkt. Dungange, amesema kati ya fedha hizo, Sh bilioni 143.43 zilikuwa zimefikia muda wa marejesho, ambapo Sh bilioni 130.04, sawa na asilimia 91, zilikuwa tayari zimerejeshwa.

Aidha, amesema Serikali tayari imeweka mwongozo unaowataka wataalamu wa fedha, maendeleo ya jamii na wataalamu wengine waliopo katika halmashauri kushiriki katika kuwaelimisha na kuwasimamia wajasiriamali wanaoomba mikopo hiyo.

Amesema mwongozo huo pia umeweka utaratibu wa kutoa mafunzo ya masuala ya fedha na ujasiriamali kwa vikundi vinavyoomba mikopo, hatua inayolenga kuwajengea uwezo wa kutumia vizuri fedha wanazokopa na kuongeza uwezekano wa mafanikio katika shughuli zao.

“Serikali itaendelea kuboresha utoaji wa mikopo ya asilimia 10 kwa wajasiriamali kwa kuwatumia wataalamu wa mafunzo ya biashara ili kuongeza ufanisi wa mikopo hiyo,” alisema Dkt. Dungange.


Na Janeth Raphael -MichuziTv


SERIKALI kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) imeendelea kuweka mkazo katika utekelezaji wa miradi ya umeme inayolenga kuhakikisha wawekezaji katika sekta mbalimbali, ikiwemo madini, viwanda, kilimo cha kisasa na ufugaji, wanapata nishati ya uhakika kwa ajili ya kuongeza uzalishaji na kuchochea ukuaji wa uchumi.


Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Nishati, Salome Makamba, wakati wa hafla ya utiaji saini mkataba wa utekelezaji wa mradi wa kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 220 pamoja na kituo cha kupokea na kupoza umeme cha kilovoti 220/33 kwa ajili ya Geita Gold Mining (GGM), iliyofanyika jijini Dodoma.

Makamba amesema Serikali inalenga kufanya upatikanaji wa nishati ya uhakika kuwa miongoni mwa vivutio vikubwa vya uwekezaji nchini, kwa kuhakikisha miundombinu ya umeme inaendana na mahitaji ya uchumi na kasi ya uwekezaji.

Amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan itaendelea kuwekeza katika miundombinu ya nishati ili umeme uwe kichocheo cha uzalishaji na kivutio kwa wawekezaji zaidi kuja nchini.

“Mwekezaji anapokuja Tanzania, nishati iwe kichocheo na kivutio kikubwa cha uwekezaji na uzalishaji wake,” amesema Makamba.

Amesema Serikali pia imechukua hatua za kuimarisha uwezo wa TANESCO kifedha na kiutendaji ili shirika hilo liweze kuendelea kutekeleza miradi mikubwa ya nishati. Kwa mujibu wa Makamba, Wizara ya Fedha imeidhinisha TANESCO kukopa Sh bilioni 229.3 kutoka benki za ndani kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya kimkakati yenye lengo la kuongeza mapato na kujenga uwezo wa shirika kuendelea kuwekeza.

Amesema uwekezaji huo unalenga kuhakikisha miradi ya umeme inaleta manufaa kwa pande zote, ambapo Serikali inawekeza katika miundombinu, mwekezaji anaongeza uzalishaji, TANESCO inaongeza mapato na Taifa linapata manufaa ya kiuchumi.

Makamba amesema mradi wa GGM ni mfano wa utekelezaji wa falsafa hiyo, kwa kuwa Serikali inawekeza katika miundombinu ya umeme huku mwekezaji akitarajiwa kuongeza uzalishaji, jambo litakalosaidia kuongeza mapato ya TANESCO na Serikali pamoja na kuchochea shughuli nyingine za kiuchumi.

Amesema uwekezaji katika nishati hauhusiani tu na kuwasha taa au kuendesha mashine, bali una nafasi kubwa katika kuongeza uzalishaji, kupunguza gharama za uzalishaji, kuongeza ajira, mapato ya Serikali, thamani ya rasilimali za nchi na kuvutia wawekezaji wengine.

“Tunapozungumzia uwekezaji katika nishati, tunazungumzia zaidi ya kuwasha taa au kuendesha mashine. Tunazungumzia kuongeza uzalishaji, kupunguza gharama za uzalishaji, kuongeza ajira, kuongeza mapato ya Serikali, kuongeza thamani ya rasilimali zetu na kuvutia wawekezaji wengine kuja kuwekeza nchini,” amesema.

Makamba amesema kila njia ya umeme inayojengwa, kila kituo kinachokamilishwa na kila mwekezaji anayeunganishwa kwenye Gridi ya Taifa ni sehemu ya kujenga uchumi imara, endelevu na wenye ushindani.

Amesema Wizara ya Nishati itaendelea kusimamia utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050 inayotambua nishati kuwa miongoni mwa vichocheo muhimu vya ukuaji wa uchumi na maendeleo ya nchi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Geita, Hashim Komba, ameishukuru Serikali chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa inayoendelea katika kuimarisha sekta ya nishati, akisema nishati ni eneo muhimu linalochochea maendeleo ya sekta nyingine za uzalishaji.

Komba amesema mkoani Geita kazi ya kusambaza umeme inaendelea, huku akipongeza TANESCO kwa namna inavyoendelea kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kugusa moja kwa moja sekta ya madini ambayo ni miongoni mwa sekta muhimu katika mkoa huo.

Amesema ongezeko la shughuli za utafiti wa madini limechochea kuongezeka kwa maeneo ya uchimbaji, hali inayosababisha mahitaji makubwa ya nishati ya uhakika kwa wachimbaji wakubwa, wa kati na wadogo.

Komba amesema mradi wa kupeleka umeme GGM haupaswi kuangaliwa kwa upande wa kusaidia mgodi pekee, bali pia kwa namna unavyoweza kuchochea uwekezaji na kuongeza mapato ya Serikali, pamoja na kuwezesha wachimbaji wadogo kupata umeme wa kutosha katika maeneo yao ya shughuli.

Amesema mkoa huo utaendelea kushirikiana na TANESCO kutoa elimu kwa wachimbaji wadogo kuhusu namna wanavyoweza kutumia fursa ya umeme katika maeneo yao ya uchimbaji, hususan kupitia Maonesho ya Teknolojia ya Madini yanayofanyika kila mwaka mkoani Geita.

Kwa mwaka huu, amesema Geita inatarajia kufanya maonesho hayo kwa mara ya tisa, huku akiahidi kuwa Serikali ya Mkoa itashirikiana na TANESCO kuhakikisha wachimbaji wadogo wanaelewa vizuri fursa zinazotokana na upatikanaji wa umeme katika maeneo yao.

Komba pia amesema Serikali ya Mkoa wa Geita imejipanga kushirikiana na mkandarasi wa mradi huo kuhakikisha utekelezaji wake unakwenda kwa wakati na kwamba changamoto zozote zinazoweza kuchelewesha mradi zitashughulikiwa kwa haraka.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Lazaro Twange, amesema uwekezaji nchini unaendelea kukua, hususan katika sekta ya madini ambayo inahitaji nishati ya uhakika kutokana na matumizi ya teknolojia na mashine za kisasa.

Twange amesema upatikanaji wa umeme wa uhakika utawawezesha wachimbaji wakubwa, wa kati na wadogo kuongeza ufanisi wa shughuli zao, kutumia teknolojia za kisasa na kuongeza uzalishaji.

Amesema TANESCO itaendelea kutekeleza miradi ya umeme kwa kuzingatia mahitaji ya wawekezaji na sekta mbalimbali za uzalishaji, ili kuhakikisha nishati inakuwa kichocheo cha shughuli za kiuchumi nchini.

Mradi wa kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 220 pamoja na kituo cha kupokea na kupoza umeme cha kilovoti 220/33 kwa ajili ya GGM unatarajiwa kukamilika ndani ya miezi 18 iliyopangwa.

Serikali imeeleza kuwa uwekezaji katika miundombinu ya umeme ni sehemu muhimu ya kuongeza uzalishaji, mapato ya TANESCO, ajira na uwekezaji, huku ukichangia kwa ujumla katika ukuaji na maendeleo ya uchumi wa Taifa.











WASUSI mbalimbali nchini wameipongeza Kampuni ya Darling Hair kwa kuwawezesha kiuchumi na kuwakwamua kutoka kwenye umaskini kupitia programu yake maalumu inayofahamika kama Loyalty.

Pongezi hizo zilitolewa katika hafla maalumu iliyofanyika Sinza, Jijini Dar es Salaam na kuwakusanya mamia ya wasusi katika hafla maalumu ya kupongezana na kutoa zawadi mbalimbali iliyoandaliwa na Darling Hair na kuhudhuriwa na uongozi wa juu kabisa wa kampuni hiyo.

“Kupitia program hii Darling Hair imetusaidia sana sisi kama wasusi na wenye masaluni kwani sasa hivi hatununui vifaa hasa viti. Tunakusanya lebo za bidhaa mbalimbali za Darling Hair na kujikusanyia pointi mbalimbali zinazotuwezesha kushinda zawadi mbalimbali,” alisema Veronica Millinga, mmoja wa wasusi aliyehudhuria hafla hiyo.

Alitoa wito kwa wasusi ambao hawajajiunga na program hiyo kuchangamkia fursa hiyo kwani faida zake ni nyingi ikiwemo baadhi ya wasusi wadogo kufungua saluni zao wenyewe.

Naye Ramadhani Kataya ambaye ni msusi na mmiliki wa saluni, alisema kupitia programu hii Darling Hair imejiweka karibu sana na wateja wake na inafuatilia hatua kwa hatua ili kuhakikisha wanapata huduma bora.

“Hawa Darling ni wabunifu sana hata mteja akija na hitaji fulani kwa haraka tu unafahamu kuwa Darling Hair wana suluhisho na ukiwapigia wanakuhudumia haraka,” alisema.

Rukia Adam, ambaye pia ni msusi, alisema program hiyo ya Loyalty imewasaidia wasusi wengi wadogo na kuwafanya wajiamini zaidi kwa kuwapa mitaji ya vifaa mbalimbali vya saluni.

“Kwa kweli wametuwezesha sana na tunaomba programu hii iwe ya kudumu ili wengi zaidi wafadike na pia itunyanyue kutoka hatua moja kwenda hatua nyingine,” alisema.

Meneja Saluni wa Darling Hair, Joyce Mwijage, alisema, awamu ya kwanza ya programu hiyo ilipata mafanikio makubwa ambapo idadi ya wasusi iliongezeka kutoka 5000 hadi 15,000.

Alisema hafla hii iliyowakusanya wasusi kutoka Tegeta, Wazo, Makonde, Boko, Bunju, Tanki Bovu, Mivumoni, Kunduchi na Kawe ni ya pili tangu kampuni hiyo izindue awamu ya pili ya program hiyo iliyoanza 2024. “Baada ya Dar es Salaam tutaenda mikoa mbalimbali ili tuwafikie wasusi nchi nzima,” alisema.

Alisema washiriki walikusanya lebo za bidhaa za Darling Hair na kujizolea pointi kadhaa ambazo ziliwawezesha kujipatia zawadi mbalimbali.

“Lengo la program hii ya Loyalty ni kuwazawadia wasusi wadodo wadogo ili waweze kujiendeleza na hatimaye kufungua saluni zao wenyewe kutokana na vifaa vya saluni wanavyojishindia kwa kukusanya lebo za bidhaa zetu na kujizolea pointi kwa kila lebo.”Alisema.

Aliongeza kuwa baada ya Dar es Salaam.watahamia katika mikoa mingine ambapo amewataka wasusi hao kujipanga kwa kampeni hiyo ambayo kwa mujibu wa meneja huyo, ni ya kudumu.

Kulikuwa na zawadi, michezo mbalimbali, mziki uliopambwa na wasanii mbalimbali akiwemo msanii maarufu, Click Master ambaye hakuwaangusha mashabiki wake kwa kuimba nao nyimbo kama Watajua na Sherehe.


▪️︎ Azindua Mfumo wa Kitaifa wa Taarifa za Uwezeshaji Kiuchumi (NEMIS)

▪️︎ Ataka wigo wa miradi kwa Watanzania kupanuliwa

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, ametoa wito wa kuhakikisha Watanzania wanashiriki kikamilifu katika uchumi wa nchi yao, akisisitiza kuwa uwezeshaji wa wananchi ni msingi wa kuongeza ajira, kukuza sekta binafsi, kuongeza mapato na kupunguza umaskini.

Dkt. Mwigulu ameyasema hayo leo (Alhamisi, Septemba 03, 2026) wakati akifungua Kongamano la Tano la Taifa la Ushiriki wa Watanzania katika Masuala ya Uchumi, lililofanyika Dodoma, lenye kaulimbiu inayosisitiza ushiriki wa Watanzania kama nguzo ya uchumi shindani na jumuishi kuelekea Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Amesema Serikali chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuweka mazingira ya kisera, kisheria na kiutendaji yatakayowawezesha Watanzania kushiriki moja kwa moja katika shughuli za kiuchumi, akisisitiza kuwa lengo si kuwazuia wawekezaji wa nje bali kuongeza uwezo na ushiriki wa Watanzania.

“Tuwawezeshe Watanzania kushika uchumi wao. Hii ndiyo njia ya kuongeza ajira, kuongeza vyanzo vya mapato na kujenga sekta binafsi yenye nguvu,” amesema.

Dkt. Mwigulu amesema Tanzania ina rasilimali nyingi na fursa kubwa za kiuchumi, hivyo ni muhimu kuhakikisha fursa hizo zinatafsiriwa kuwa ajira, biashara, uwekezaji na umiliki kwa Watanzania.Dkt. Mwigulu ameiagiza Wizara ya Fedha kuhakikisha marekebisho yanayofuata ya sheria za ununuzi yanaongeza wigo wa miradi inayoweza kutekelezwa na kampuni za Kitanzania.

Amesema kiwango cha Shilingi bilioni 50 kwa baadhi ya miradi kimekuwa kidogo kutokana na kukua kwa uchumi na uwezo wa kampuni za ndani, hivyo akapendekeza kiwango hicho kipandishwe hadi zaidi ya Shilingi bilioni 100 au Shilingi bilioni 150.

“Hii ya bilioni 50 imeshakuwa ya kawaida. Wekeni bilioni 100... au kama mnarekebisha sasa ikachukua muda, wekeni bilioni 150. Mambo yanaenda mbele. Tuwawezeshe Watanzania kushika uchumi wao,” amesema.

Amesisitiza pia kuwa fursa zinazotolewa na Serikali zinapaswa kutumiwa kwa uwajibikaji, akizitaka kampuni za Kitanzania kuhakikisha fedha za miradi zinatumika kutekeleza kazi kwa kiwango na ubora unaostahili, na kuonya kuwa Serikali haitasita kuchukua hatua dhidi ya watakaotumia vibaya fedha za umma.

Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu amezindua rasmi Mfumo wa Kitaifa wa Taarifa za Uwezeshaji Kiuchumi (NEMIS) unaolenga kurahisisha upatikanaji wa taarifa kuhusu fursa mbalimbali za uwezeshaji kwa Watanzania.

Mfumo huo utasaidia kuwafikishia wananchi taarifa kuhusu fursa za mitaji kupitia mifuko na programu za uwezeshaji, zabuni za umma, fursa za uwekezaji pamoja na taarifa nyingine muhimu za kiuchumi.Dkt. Mwigulu amehitimisha kwa kusisitiza umuhimu wa kuondoka kwenye mipango na sheria na kuelekea kwenye utekelezaji unaoleta matokeo kwa wananchi.

“Tanzania inasifika sana kwa mipango mizuri, inasifika sana kwa sheria hizi hizi tunazoziandika. Sasa tupige hatua twende kwenye kuhakikisha haya tunayotekeleza, haya tunayopanga, haya tunayoyaandika yanaonekana kwenye vitendo.”

Akizungumza katika kongamano hilo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Prof. Palamagamba Kabudi, amesema Serikali imeendelea kuweka mifumo, sera na sheria zinazolenga kuongeza ushiriki wa Watanzania katika uchumi, akisisitiza umuhimu wa uratibu ili fursa hizo ziwafikie wananchi na kuongeza ushiriki wao katika shughuli za kiuchumi.

Kwa upande wake, Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, amesema manunuzi ya bidhaa na huduma katika sekta ya madini yanafikia Shilingi trilioni 5.1 kwa mwaka, ambapo Serikali imehakikisha asilimia 90 ya manunuzi hayo yanabaki nchini Tanzania, hatua inayoongeza ushiriki wa Watanzania katika mnyororo wa thamani wa sekta hiyo.

Kwa niaba ya Bunge, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Edwin Swale, amesema Bunge limeendelea kuunga mkono hatua za Serikali za kuwawezesha wananchi kiuchumi kupitia maboresho ya sheria, akibainisha kuwa Serikali imeweka mifuko zaidi ya 74 ya uwezeshaji na imeendelea kuchukua hatua za kupunguza vikwazo kwa wafanyabiashara na wajasiriamali.

Nae, Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Uwezeshaji Kiuchumi, Prof. Aurelia Kamuzora, amesema uwezeshaji wa wananchi unapaswa kwenda sambamba na kujenga uwezo wa watu, upatikanaji wa mitaji, taarifa na ujuzi ili Watanzania waweze kushindana ndani na nje ya nchi.

Amesema Baraza limeweka mkazo katika kuwafikishia wananchi taarifa za fursa za kiuchumi na kuimarisha vituo vya uwezeshaji katika mikoa na wilaya.













-Yazindua bidhaa tatu za Jubilee Life Insurance ambazo ni Fanaka Plus, Smart Education Insurance Plan na Akiba Flex Plan


Na Said Mwishehe, Michuzi TV

MAMLAKA ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) imezitaka kampuni za bima kubuni bidhaa zinazotoa majibu ya vitendo kwa changamoto zinazowakabili wananchi, ikisema ubora wa bidhaa za bima haupaswi kupimwa kwa idadi ya watu waliojiunga pekee.

Kamishna wa Bima, Dk.Baghayo Saqware amesema kampuni zinazolenga kuongeza ujumuishi wa kifedha zinapaswa kwanza kuelewa mazingira wanamoishi Watanzania na changamoto zinazowakabili kabla ya kubuni bidhaa zinazokidhi mahitaji yao.

Dk.Saqware ametoa kauli hiyo katika hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Mkurugenzi wa Uzingatiaji wa Sheria na Kanuni wa TIRA, Bw Alex Rock wakati wa uzinduzi wa bidhaa tatu mpya za bima ya maisha za Jubilee Life Insurance Tanzania uliofanyika leo Septemba 3,2026 jijini Dar es Salaam.

“Mwito wangu kwa Jubilee Life Insurance na kampuni nyingine za bima ni kuendelea kubuni bidhaa zinazotoa majibu kwa changamoto za wananchi na kuboresha maisha yao,” amesema Dk Saqware.

“Ubora wa bidhaa haupimwi kwa idadi ya watu waliojiunga pekee. Uelewa hujenga imani, na imani huongeza matumizi endelevu ya bima,”amesema na kuongeza Tanzania inaingia katika hatua muhimu ya kujenga familia zenye uwezo wa kustahimili misukosuko ya kifedha na taifa lenye uimara wa kifedha huku bima ya maisha ikiwa na nafasi muhimu katika kulinda wananchi na kusaidia mipango yao ya muda mrefu.

Katika hafla hiyo, Dk.Saqware amezindua bidhaa tatu za Jubilee Life Insurance ambazo ni Fanaka Plus, Smart Education Insurance Plan na Akiba Flex Plan, zilizobuniwa kusaidia wananchi katika uwekaji akiba, maandalizi ya elimu, ulinzi wa maisha na mahitaji mengine ya kifedha ya baadaye.

Ameongeza Jubilee Life Insurance kwa kuwasilisha bidhaa hizo kwa lugha ya Kiswahili, akisema matumizi ya lugha inayoeleweka kwa urahisi ni muhimu katika kuongeza uelewa na ujumuishi katika huduma za bima.

“Matumizi ya lugha inayoeleweka katika kutoa taarifa na elimu kuhusu bima huwawezesha wananchi kuelewa kwa usahihi faida, masharti na wajibu wao kabla na baada ya kujiunga na bima,” alisema.

Dk.Saqware amesema pia bima ya maisha ni nyenzo muhimu katika kujenga usalama wa kifedha na uwezo wa kustahimili changamoto kwa mtu binafsi, familia na taifa kwa ujumla.

Amesisitiza bima hiyo hulinda kipato na mipango ya maisha dhidi ya athari za kifo, ulemavu, maradhi, ajali na matukio mengine yasiyotarajiwa, huku pia ikiwasaidia wananchi kuweka akiba kwa ajili ya mahitaji muhimu ya baadaye, yakiwemo elimu ya watoto na ustawi wa familia.

“Bila ulinzi wa bima, tukio lisilotarajiwa linaweza kukatisha elimu ya watoto, kuathiri maisha ya familia na hata kuzima ndoto za wanufaika,” alisema.Kupitia bima ya maisha, ndoto na mipango hiyo inaweza kulindwa na kuendelea kuwa halisi.”

Pia amesema matumizi ya bima ya maisha nchini bado hayajafikia kiwango kinachotarajiwa, huku baadhi ya sababu zikitajwa kuwa ni aina na muundo wa bidhaa zinazopatikana sokoni pamoja na uwezo wake wa kujibu mahitaji halisi ya wananchi.

Pamoja na hayo amesema uzinduzi wa bidhaa hizo unaendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kujenga uchumi imara, jumuishi na wenye uwezo wa kustahimili misukosuko.

Amesema hatua hiyo pia inaunga mkono Mpango Mkuu wa Maendeleo ya Sekta ya Fedha wa mwaka 2020–2030, ambao unalenga kuongeza mchango wa bima ya maisha katika pato la taifa hadi kufikia asilimia 3 ifikapo mwaka 2030.

Kwa upande wake Ofisa Mtendaji Mkuu wa Jubilee Life Insurance Tanzania Helena Mzena amesema kampuni hiyo imeendelea kuboresha bidhaa zake ili kuwapatia wateja thamani na uhakika zaidi.

Amesema Fanaka Life Plan imeboreshwa na kubadilishwa jina kuwa Fanaka Plus, ikiwapa wateja fursa ya kukuza fedha zao huku wakipata ulinzi wa maisha na amani ya moyo.

Ameongeza kuwa Akiba Flex inawapa wateja uhuru zaidi wa kuweka michango na kufanya miamala ya fedha kulingana na mahitaji yao.

Aidha, amesema Smart Education Insurance Plan imeundwa mahsusi kuwasaidia wazazi na walezi kujiandaa kwa ajili ya elimu ya watoto wao.“Hapa, mteja anaweza kuweka akiba ili kuhakikisha ndoto za kielimu za watoto wake zinatimia, huku pia akiwa na ulinzi wa maisha.

“Bidhaa hizi za bima ni ushahidi kwamba tunajali na kuthamini ndoto za wateja wetu na tunataka kuhakikisha ndoto hizo zinatimia bila msongo usio wa lazima.”

Wakati huo huo Mwenyekiti wa Bodi ya Jubilee Insurance Amyn Lalji amesema uzinduzi huo ni hatua nyingine muhimu katika safari ya Jubilee Life Insurance Tanzania na unaakisi dhamira ya kampuni hiyo ya kutoa suluhisho bunifu na la vitendo linalokidhi mahitaji yanayobadilika ya Watanzania.





Na Mwandishi Wetu

MAKAMU wa Rais wa Tanzania, Deogratius Ndejembi, ametoa maeekezo kwa Wizara ya Viwanda na Biashara kukaa meza moja na wazalishaji wa saruji nchini ili kuweka mikakati ya haraka itakayohakikisha saruji inapatikana kwa wingi na bei nafuu.

Ametoa maelekezo jijini Dar es Salaam alipokuwa katika hafla ya utoaji wa Tuzo za Rais kwa Mzalishaji Bora Viwandani (President’s Manufacturer of the Year Awards - PMAYA), zinazoratibiwa na Shirikisho la Wenye Viwanda Tanzania (CTI).

Akieleza kero ya wananchi kuhusu gharama za ujenzi, Makamu wa Rais amesema kwamba wananchi wanalazimika kununua saruji kwa bei kubwa kutokana na usimamizi na uratibu dhaifu wa uzalishaji viwandani, jambo ambalo linaenda kinyume na maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Kutokana na bei ya saruji kuwa juu Makamu wa Rais Ndejembi amesema” Nakuagiza Waziri wa Viwanda na Biashara, Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda pamoja na Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), kaeni mmalize hili suala ili mwananchi apate saruji kwa bei iliyokuwepo awali.

Amesisitiza baada ya Wizara hiyo kukaa anataka kupata ripoti kuhusu jambo hilo huku akiwataka wajadili na kisha mwandike ripoti ambayo itakabidhiwa kwa Rais Dk.Samia Suluhu Hassan.


Na Mwandishi Wetu.

Dar es Salaam, Septemba 3, 2026: Wananchi wamehimizwa kujitokeza kwa wingi kupigia kura kazi 294 za uandishi wa habari na makala za maendeleo zilizofuzu katika Samia Kalamu Awards 2026.

Wito huo umetolewa leo, Septemba 3, 2026, na Mwakilishi wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa habari (JAB) Prudence Constantine, wakati wa mkutano wa kutangaza kuanza kwa zoezi la upigaji kura litakalodumu hadi Septemba 30, 2026.

Prudence amesema kura za wananchi ni sehemu muhimu ya mchakato wa kumpata mshindi, kwa kuwa zinatoa nafasi kwa jamii kutambua na kuunga mkono kazi zilizoleta mchango au athari chanya katika maisha ya watu na maendeleo ya Taifa.

Amesema wananchi, wakiwa watumiaji wa maudhui ya habari, wana nafasi ya kuchagua kazi wanazoona zimefanya vizuri, zimeakisi mahitaji na maslahi ya jamii na kusaidia kuibua au kuelimisha kuhusu masuala muhimu ya maendeleo.

Wananchi wanaweza kupiga kura kupitia tovuti ya www.samiaawards.tz na kufuata maelekezo yaliyowekwa ili kuchagua kazi wanayoipendelea.

Pia, kura zinaweza kupigwa kupitia ujumbe mfupi wa maandishi kwa kutuma neno “SKA”, likifuatiwa na namba ya mshiriki kwenda 15200.

Akizungumza kuhusu Kazi 294 zilizofuzu kupigiwa kura Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Mhandishi Peter Mwasalyanda amesema kazi hizo zimefuzu baada ya tathmini ya kazi 3,003 zilizowasilishwa na waombaji 985. Jopo la majaji lilifanya tathmini kwa kuzingatia vigezo vilivyowekwa na kuteua kazi zilizopata alama za juu.

Naye Mwenyekiti Mwenza wa Mashindano hayo na Mkurugenzi wa TAMWA, Dkt. Rose Reuben, amesema mashindano hayo yamewaleta pamoja waandishi wa habari kutoka maeneo ya vijijini na mijini, akisisitiza kuwa washiriki watashindana kwa kuzingatia ubora wa kazi zao na si umaarufu wao.

Kwa mujibu wa mmoja wa majaji wa mashindano hayo, Bi. Beatrice Bandawe, amesema kuwa miongoni mwa maeneo yaliyopatiwa kipaumbele katika kazi zilizowasilishwa ni pamoja na afya, jinsia na makundi maalum, mazingira pamoja na elimu.

Samia Kalamu Awards zinaandaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA kwa Kuhsirikiana na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) pamoja na Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) zikilenga kutambua, kuenzi na kuhamasisha ubora, weledi na ubunifu katika uandishi wa habari na utayarishaji wa makala za maendeleo nchini.





VIJANA 50 wenye ufaulu wa juu lakini wanaotoka katika familia zenye uwezo mdogo wa kifedha watanufaika na uwezeshaji wa elimu ya chuo kikuu na maandalizi ya kuingia katika soko la ajira.

NMB Foundation (NMBF), ikishirikiana na Benki ya NMB, imetenga Sh bilioni 1 kuwawezesha vijana hao kupitia dirisha la tatu la programu ya Nuru Yangu Scholarship and Mentorship kwa mwaka wa masomo 2026/27.

Maombi yote yatapokelewa kupitia tovuti ya NMB Foundation, foundation.nmbbank.co.tz, kuanzia leo hadi tarehe 18 Septemba 2026.

Programu hiyo inalenga Watanzania waliomaliza Kidato cha Sita mwaka huu kwa Daraja la Kwanza lenye pointi tatu hadi tano. Waombaji pia wanapaswa kuwa na ushahidi wa uhitaji wa kifedha na kutarajia kujiunga na taasisi za elimu ya juu zinazotambuliwa nchini.

Akizungumza jijini Dar es Salaam, Meneja Mkuu wa NMB Foundation, Nelson Karumuna, alisema vijana watakaochaguliwa wataungana na wanufaika 101 waliowezeshwa kupitia awamu mbili zilizopita.

Kwa kuongezwa vijana hao 50, idadi ya wanufaika wa programu hiyo itafikia 151. NMBF imetumia zaidi ya Sh bilioni 2.1 katika awamu zilizopita, huku Sh bilioni 1 zikitengwa kwa kundi jipya.

“Uwezeshaji huu utagharamia ada, fedha za kujikimu, mafunzo kwa vitendo, malipo ya lazima ya chuo na vifaa vya kujifunzia, ikiwemo kompyuta mpakato,” alisema Karumuna.

Alisema vijana watakaopatikana pia watapatiwa malezi na ushauri wa kitaaluma, mafunzo ya uongozi, maandalizi ya kuingia katika soko la ajira na fursa za kujifunza kwa vitendo.

Karumuna alisisitiza kuwa maombi hayana gharama na hakuna mtu wala taasisi iliyopewa mamlaka ya kuuza nafasi hizo. Uchaguzi utafanywa kwa kuzingatia vigezo vilivyowekwa na uhakiki wa kina ili kuhakikisha fursa zinawafikia walengwa.

Programu ya Nuru Yangu ilianzishwa Mei 19, 2022, ikiwa na lengo la kuondoa vikwazo vya kifedha vinavyowazuia vijana wenye uwezo mkubwa kitaaluma kuendelea na elimu ya juu.

Mmoja wa wanufaika wake, Elia Johnson Kaberege, aliyehitimu Shahada ya Uhasibu katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mwaka 2025, alisema programu hiyo ilimwezesha kumudu gharama za masomo na mahitaji mengine ambayo familia yake isingeweza kugharamia.

Naye Irene John Busorwa, mhitimu wa Chuo Kikuu Mzumbe, alisema alikaribia kukosa nafasi ya kujiunga na chuo kutokana na hali ya kifedha ya familia yake. Kupitia Nuru Yangu, aliweza kusoma kwa miaka mitatu na kuhitimu. Kwa sasa ameajiriwa katika kampuni ya ukaguzi wa hesabu.

NMBF, ikishirikiana na Benki ya NMB, imewataka vijana wenye sifa kutuma maombi kupitia tovuti rasmi pekee kabla ya kufungwa kwa dirisha hilo Septemba 18, 2026.





Na mwandishi wetu

Makamu wa Rais Deogratius Ndejembi akimkabidhi tuzo Msemaji wa Kampuni ya Alliance One Wakili John Magoti(kulia), ambaye kampuni yake imetwaa nafasi ya Mshindi wa Pili wa Jumla wa Tuzo za Rais za Mzalishaji Bora wa mwaka pamoja na mshindi wa Kwanza wa Sekta ya Uchakataji Tumbaku, huku Waziri wa Viwanda na Biashara Wakili Judith Kapinga akishuhudia.

Makamu wa Rais Degratius Ndejembi amewaasa wazalishaji wa viwanda nchini kuhakikisha uzalishaji wa bidhaa nchini, unalenga kuwapunguzia mzigo wa gharama za maisha watanzania.

Amesema hayo kwenye hafla ya utoaji wa Tuzo za 19 za Rais za Wazalishaji bora za mwaka huu, ambapo Makamu wa Rais amemwakilisha Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan.Katika tuzo hizo kampuni ya tumbaku ya Alliance One, imekuwa kinara wa tuzo hizo kwa kushika nafasi ya mshindi wa pili wa jumla ya tuzo zote, lakini pia imeshinda tuzo ya mzalishaji bora wa uchakatataji tumbaku.
Akitoa mfano amesema wazalishaji wa simenti nchini wanapaswa kuongeza ushirikiano kata yao na wauza malighafi, ikiwemo klinka na malighafi nyingine, lengo likiwa kushusha gharama bidhaa hiyo, sambamba na maelekezo ya Rais kwamba wananchi waipate bidhaa hiyo kwa bei ya awali ambayo ilikuwa ni ndogo.

 “Katika kukuza uchumi na kuboresha maisha ya Watanzania, sekta ya viwanda ina nafasi kubwa sana,na duniani kote sekta ya viwanda ndiyo chimbuko la mandeleo ya haraka mhimiri mkuu wa uongezaji thamani wa malighafi zilizopo nchini na mtoaji wa ajira kwa wananchi na kuongeza mapato ya serikali pampja na fedha za kigeni,”amesema.

Ameipongeza kauli mbiu tuzo hizo mwaka huu ambayo ni kuhamasisha uendelevu,uwajibikaji na ustahimilivu katika uzalishaji viwandani, kwani inanenda sambamba na dira ya maendeleo ya taifa ya mwaka 2050 ikichagiza na kuchochea mageuzi endelevu ya viwanda hapa nchini.

 “Kutokana na wingi wa raslimali tulizonazo hapa nchini ikiwemo misitu na madini mbalimbali ni muhimu kukuza sekta ya viwandana kuendelea kujenga mahusiano na sekta ya viwanda na sekta nyingine ili kuongeza ufanisi na kuharakisha maendeleo jumuishi na hatimaye kuongeza kipato cha watanzania walio wengi,”amesema.

Amesema serikali za inatambua na kuunga mkono juhudi za sekta ya uzalishaji nchini, kwani kutokana na hilo, mchango wa sekta uzalishaji viwandani kwenye pato la taifa mwaka 2025 ulifikia asilimia 5.9 na pia asilimia 12 mpaka 22 ya bidhaa zilizouzwa nje ya nchi kwenye mwaka huo zilikuwa za viwandani.

Hata hivyo aliwaasa wenye viwanda nchini kuongeza uzalishaji hatimaye waweze kupenya na kukabiliana na ushindani kwenye masoko ya nchi jirani na siyo kuzalisha bidhaa za soko la hapa nchini peke yake.

Akiongea baada ya kupokea tuzo hiyo, Msemaji wa Alliance One Wakili John Magoti ameishukuru serikali ya awamu ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuweka mazingira mazuri ya kazi na biashara nchini yanayowezesha uwekezaji katika uzalishaji bora na endelevu.

“Sisi Alliance One tumeipokea tuzo hii kwa bashasha sana tukiamini kwamba imepatikana kutokana na uwajibikaji wa pamoja kati yetu sisi wafanyakazi wa kudumu wapatao 350 pamoja na wale msimu 4,600 na wadau wengine ambao ni wakulima wa tumbaku zaidi ya laki moja, na kiukweli tuzo hii ni yetu sote kwa pamoja,” amesema.

Amesema kampuni hiyo imeboresha uzalishaji ikiwemo matumizi ya umeme jua kiwandani nyakati za mchana na pamoja na matumizi ya gesi asilia kwenye magari na baadhi ya mitambo kiwandani hapo.

“Tumefanya hivyo ili kwenda sambamba na mdundo wa dunia ambao ni utunzaji wa mazingira na upunguzaji wa gesi ya ukaa wakati huo huo tukiongeza tija na kuokoa baadhi ya gharama ambazo sasa tunazirejesha kwa wananchi kama misaada kwa jamii ambapo kila mwaka tunatenga zaidi ya milioni 500 kusaidia jamii kwenye elimu,maji na mazingira,” amesema.

Washindi wengine wa Tuzo za 19 za Mzalishaji bora ni Sili Africa ambaye ni mshindi wa Jumla huku Kiwanda cha Sigara kikishika nafasi ya Tatukwenye tuzo hizo zinazoratibiwa na Shirikisho la wenye viwanda Tanzania (CTI).

Akongea kwenye hafla hiyo, Mwenyekiti wa CTI Sufian Ally ameiomba serikali kuongeza mapambano dhidi ya bidhaa bandia zinazoathiri soko la bidhaa za viwandani.

Aidha, ameiomba serikali kuendelea kuweka mazingira ya mazuri ya uzalishaji ikiwemo kupunguza gharama za uzalishaji kwa kutazama upya gharama za umeme,kumaliza tatizo la ucheleweshaji wa uondoaji bidhaa kutoka bandarini,pamoja na ushiriki wa kampuni za kitanzania kwenye tenda mbalimbali mambo ambayo Makamu wa Rais amesema serikali inaenda kuyafanyia kazi.

 




Na Mwandishi Wetu
OFISI ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR-TAMISEMI) imeanza kuwajengea uwezo walimu wa shule za sekondari za Serikali katika Jiji la Arusha na Halmashauri ya Arusha kuhusu matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika ufundishaji, ujifunzaji na upimaji wa wanafunzi.

Mafunzo hayo ya siku nne yanayofanyika katika Hoteli ya Gold Crest jijini Arusha kuanzia Septemba mosi hadi nne, 2026, yanafanyika kwa ushirikiano kati ya OR-TAMISEMI, Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) na Taasisi ya Elimu Tanzania (TIE).

Mafunzo hayo yanaendeshwa kupitia Mradi wa ICT Transforming Education in Africa – Awamu ya Tatu, unaoungwa mkono na Mfuko wa Korean Funds-in-Trust (KFIT), kwa lengo la kuwapatia walimu ujuzi wa vitendo wa kuunganisha TEHAMA katika ufundishaji, ujifunzaji na upimaji.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mkurugenzi Msaidizi wa Elimu kutoka OR-TAMISEMI, Melchiory Baltazary, alisema Serikali imejipanga kuendelea kuimarisha uwezo wa walimu kutumia TEHAMA kwa ufanisi ili kuboresha ubora wa elimu nchini.

Alisema ushirikiano kati ya Serikali, UNESCO na TIE umekuwa muhimu katika kuwapatia walimu ujuzi wa vitendo ambao wanaweza kuutumia moja kwa moja katika shughuli za ufundishaji na ujifunzaji.

Baltazary aliwataka walimu hao kutumia kikamilifu maarifa wanayoyapata na kuyasambaza kwa walimu wenzao ambao hawakupata nafasi ya kushiriki mafunzo hayo.

Alisema mfumo wa mafunzo wa kueneza ujuzi (cascade training) utasaidia kuwafikia walimu wengi zaidi katika shule na halmashauri zao.

Pia aliwahimiza walimu kuendelea kutumia mifumo na rasilimali za kidijitali zinazotolewa na Serikali ili kuimarisha uwezo wao kitaaluma hata baada ya kumalizika kwa mafunzo ya ana kwa ana.

Kwa upande wake, Mkuu wa Sekta ya Elimu katika Ofisi ya UNESCO Dar es Salaam, Dkt. Faith Shayo, alisema uimarishaji wa ujuzi wa kidijitali kwa walimu ni muhimu ili kuhakikisha mfumo wa elimu unaendana na kasi ya mabadiliko ya teknolojia.

Dkt. Shayo aliwataka walimu hao kushirikisha wenzao maarifa na ujuzi wanaoupata ili kuongeza idadi ya walimu wanaoweza kutumia TEHAMA katika elimu

Alisema walimu wana nafasi kubwa katika mabadiliko ya elimu kwa kuwa ndio wanaohakikisha teknolojia na ubunifu vinatafsirika kuwa mbinu bora za ufundishaji ndani ya madarasa.

“Tunatarajia mtashirikisha walimu wenzenu mnayojifunza hapa ili nao waweze kwenda sambamba na mabadiliko haya katika elimu,” alisema.

Aliongeza kuwa teknolojia inapaswa kutumika kuboresha ubora wa ufundishaji na ujifunzaji, kuongeza upatikanaji wa maarifa na kuwawezesha wanafunzi kupata ujuzi unaohitajika katika karne ya 21.

Naye Afisa Taaluma wa Mkoa wa Arusha, Oscar Kapinga, alisema matumizi sahihi ya teknolojia yanaweza kurahisisha ufundishaji na ujifunzaji pamoja na kuongeza fursa kwa wanafunzi kupata maarifa na rasilimali mbalimbali za kielimu.

Aliwataka walimu kuhakikisha matumizi ya TEHAMA yanaelekezwa katika maeneo yanayochangia moja kwa moja kuboresha matokeo ya ujifunzaji.

Mafunzo hayo yanahusisha maeneo mbalimbali ya ujuzi wa kidijitali, ikiwamo matumizi ya zana na majukwaa ya kujifunzia kidijitali, matumizi ya TEHAMA katika ufundishaji na upimaji, Rasilimali Huria za Kielimu (OER), utafutaji wa taarifa mtandaoni na matumizi ya teknolojia katika utekelezaji wa mtaala.

Pia walimu wanafundishwa mbinu shirikishi za ufundishaji, usimamizi wa kumbukumbu na taarifa za shule, uandaaji wa rasilimali za kujifunzia kidijitali, utengenezaji wa maudhui ya kielimu kwa njia ya sauti na picha pamoja na matumizi ya Akili Bandia (AI) katika elimu.

Walimu hao wanatumia mfumo wa TIE wa Mafunzo Endelevu ya Maendeleo ya Kitaaluma kwa Walimu (TCPD LMS), unaounganishwa na mfumo wa Serikali wa MEWAKA, kupata vifaa vya mafunzo na kukamilisha moduli mbalimbali.

Akieleza utekelezaji wa mradi huo, Gabriela Lucas kutoka Sekta ya Elimu ya UNESCO, alisema mpango huo unaolenga kujenga uwezo wa walimu kutumia teknolojia kwa ufanisi katika ufundishaji na ujifunzaji unatumia pia mifumo iliyopo ya Serikali katika kuwawezesha walimu kuendelea kujifunza.

Alisema UNESCO inalenga kuhakikisha kila mwalimu anakuwa na uwezo wa kutumia TEHAMA katika ufundishaji na ujifunzaji.

Kwa mujibu wa Lucas, mfumo wa ICT-CSTT una viwango mbalimbali vya umahiri vinavyowawezesha walimu kukuza ujuzi wao wa kidijitali hatua kwa hatua kulingana na kiwango walichonacho.

Alisema mfumo huo una jumla ya moduli 15, huku mafunzo ya Arusha yakilenga viwango vya Mwanzo na Kati vinavyohusisha moduli 10, pamoja na utangulizi wa moduli tano za kiwango cha Juu.

Alifafanua kuwa mradi huo unatumia mfumo wa mafunzo ya kueneza ujuzi ambapo walimu wanaopata mafunzo wanatarajiwa kuwafundisha wenzao katika shule zao.

Alisema mafunzo hayo yameanza Morogoro na sasa yanaendelea Arusha, huku mradi ukitekelezwa pia nchini Namibia na Uganda.

Naye mwezeshaji kutoka TIE, Watson Mtewele, alisema moduli zinazotumika katika mafunzo hayo zinapatikana kupitia mfumo wa maendeleo endelevu ya kitaaluma kwa walimu unaojulikana kama MEWAKA.

Alisema mfumo huo unawawezesha walimu kuendelea kujifunza na kuimarisha ujuzi wao wa kitaaluma hata baada ya kumaliza mafunzo ya ana kwa ana.

Jumla ya walimu 64 kutoka Jiji la Arusha na Halmashauri ya Arusha wanashiriki mafunzo hayo na wanatarajiwa kurejea shuleni kwao na kuwasaidia walimu wenzao kutumia zana na majukwaa ya kidijitali, kuandaa maudhui ya kielimu na kutumia teknolojia katika ufundishaji, ujifunzaji na upimaji.

Mpango huo unalenga kujenga mtandao mpana wa walimu wenye ujuzi wa kidijitali kupitia mfumo wa kushirikishana na kuhamishiana maarifa na ujuzi, hatua inayotarajiwa kuwafaidisha wanafunzi.

Mafunzo hayo pia yanaunga mkono jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika elimu na kujenga nguvu kazi yenye ujuzi na maarifa yanayokidhi mahitaji ya karne ya 21.

Aidha, mpango huo unaendana na Dira ya Maendeleo ya Tanzania 2050 inayosisitiza umuhimu wa kuwa na wananchi wenye maarifa, ujuzi na uwezo wa kutumia teknolojia katika kuchochea maendeleo ya taifa.

Mafunzo hayo yanaendelea katika Hoteli ya Gold Crest jijini Arusha na yanatarajiwa kuhitimishwa Septemba 4, 2026.

Top News