Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma

Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema kuwa ni jambo la kawaida kwa baadhi ya watu kupinga hatua za Serikali, hasa pale maamuzi hayo yanapogusa maslahi yao binafsi—hususan kwa wale waliokuwa wakinufaika kwa njia zisizo halali.

Akizungumza leo jijini Dodoma mara baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa barabara ya kiwango cha lami ya Ntyuka–Mvumi–Kikombo yenye urefu wa kilomita 76, pamoja na kipande cha barabara ya Chololo–Mapinduzi (Makao Makuu ya TPDF) chenye kilomita 5, Dkt. Mwigulu alisema Serikali haitayumbishwa na kelele za wachache wanaopinga mabadiliko yenye manufaa kwa taifa.

Alieleza kuwa mara nyingi watu wanaoguswa na hatua hizo hujipanga kwa kuajiri wengine ili kuishambulia Serikali na viongozi wake kupitia mitandao au majukwaa mbalimbali ya kijamii.

“Watanzania msitishike na hao watu, kwa sababu wanafugwa huko waliko. Ili mikataba yao iendelee, ni lazima waendelee kutukana,” alisisitiza.

Dkt. Mwigulu amesema kuwa mwenendo huo si wa sasa pekee, bali umekuwepo hata katika awamu zilizopita za uongozi, ambapo baadhi ya watu walikuwa wakitoa kauli za kejeli na mashambulizi dhidi ya viongozi wanaochukua hatua thabiti.

Aidha, amebainisha kuwa hata yeye binafsi amekuwa mhanga wa mashambulizi hayo, akifananisha hali hiyo na mapambano ya kiimani, ambapo wanaosimama kupinga maovu hukumbana na upinzani mkali.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amewataka Watanzania kuendelea kumuunga mkono Rais Samia Suluhu Hassan, akisisitiza kuwa juhudi za Serikali ya awamu ya sita zinalenga kulinda rasilimali za taifa na kuhakikisha zinawanufaisha wananchi wote.

Amesisitiza kuwa miradi ya maendeleo kama ujenzi wa barabara hizo ni ushahidi wa dhamira ya dhati ya Serikali katika kuboresha miundombinu na kukuza uchumi wa nchi.





Na Mwandishi Wetu, Michuzi TV

BANK of Africa Tanzania imezindua programu ya masuluhisho na huduma mahususi za kifedha pamoja na ushauri kwa Wafanyabiashara Wadogo na wa Kati (SMEs), ikiwa ni jitihada za kuboresha upatikanaji wa mikopo, elimu ya biashara na kukuza ushindani wa biashara nchini.

Uzinduzi wa programu hiyo ulipongezwa na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Emmanuel Tutuba, aliyesema kuwa hatua hiyo inalenga kuboresha mahitaji ya kifedha ya wajasiriamali kupitia huduma, mikopo na elimu ya biashara.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi iliyofanyika katika Tawi la Lumumba jijini Dar es Salaam, Tutuba alisema tukio hilo linaashiria hatua muhimu katika kuimarisha masuluhisho ya kifedha kwa SMEs na kukuza sekta binafsi.

“Mpango huu unaonyesha mabadiliko chanya katika sekta ya benki, kutoka mfumo wa ukopeshaji wa jumla kwenda kwenye huduma jumuishi za kifedha zinazolenga mahitaji maalum ya wateja,” alisema.

Aliongeza kuwa SMEs ni uti wa mgongo wa uchumi wa Tanzania, zikichangia takribani asilimia 95 ya biashara zote na asilimia 35 ya Pato la Taifa (GDP), huku zikitoa ajira kwa zaidi ya watu milioni tano.

Aidha, alisema mpango huo unaendana na Mkakati wa Taifa wa Huduma Jumuishi za Fedha (2023–2028) unaolenga kuhakikisha Watanzania wanapata huduma za kifedha nafuu na za kuaminika. Alitaja makundi ya kipaumbele kuwa ni pamoja na wanawake, vijana, watu wenye ulemavu, wakulima na wavuvi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Bank of Africa Tanzania, Esther Cecil Maruma, alisema mkakati huo umejengwa katika uelewa wa kina wa mahitaji ya SMEs.

“Tunataka kuwezesha biashara kukua kwa kasi, kushindana vyema na kudumu kwa muda mrefu kupitia masuluhisho yanayojibu changamoto zao moja kwa moja,” alisema.

Alieleza kuwa huduma mpya zilizozinduliwa ni pamoja na ufadhili wa ankara (invoice discounting), overdraft, mikopo ya muda mfupi na mrefu, ufadhili wa mali na magari, dhamana, pamoja na huduma za biashara za kimataifa.

Maruma alisisitiza kuwa benki inalenga kuwa mshirika wa kweli wa ukuaji wa biashara, si mtoaji wa mikopo pekee.

Naibu Mkurugenzi Mtendaji – Biashara, Hamza Cherkaoui, alisema wameboresha huduma ili ziwe rahisi, zenye unyumbufu na zinazoendana na mahitaji halisi ya biashara.

Naye Mjumbe wa Bodi, Waziri Kindamba, aliipongeza benki hiyo kwa ubunifu huo unaolenga kutatua changamoto za wajasiriamali.

Kwa upande wake, mteja wa muda mrefu wa benki hiyo, Mohammed Bahasawan, alisema mpango huo ni fursa muhimu kwa wafanyabiashara kukuza mitaji na biashara zao.

“Nimekuwa mteja wa benki hii kwa miaka mingi, na ninaamini huu ni mwanzo wa suluhisho la changamoto nyingi za wajasiriamali nchini,” alisema.
Gavana wa Benki kuu ya Tanzania (BOT), Emmanuel Tutuba (katikati), akikata utepe kuzindua Programu ya masuluhisho na huduma mahususi za kifedha na ushauri kwa wafanyabiashara wa kati na wadogo (SMEs)wa Bank of Africa, jijini Dar es Salaam juzi. Kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji - Bank of Africa, Esther Cecil Maruma, Mjumbe wa Bodi - Bank of Africa - Mkurugenzi, Waziri Kindamba (kulia), Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Biashara wa benki hiyo, Hamza Cherkaoui (kushoto) na Naibu Mkurugenzi Mtendaji Uendeshaji wa Bank of Africa, Wasia Mushi.
Kaimu Mkuu wa Kitengo cha SME wa Bank of Africa, Beatrice Richard, akielezea jambo kwa Mgeni rasimi, Gavana wa Emmanuel Tutupa na Viongozi wa benki hiyo, alipotembelea eneo jipya maalum kwa wateja wa SME wakati wa uzinduzi juzi.
Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Emmanuel Tutupa na Mjumbe wa Bodi wa Bank of Africa, Waziri Kindamba na Mkurugenzi Mtendaji - Bank of Africa, Esther Cecil Maruma (kulia walio kaa) wakiwa katika picha ya pamoja na wateja wa benki hiyo, wakati wa uzinduzi wa masuluhisho na huduma mahususi za kifedha na ushauri kwa Wafanyabiashara Wadogo na wa Kati (SMEs).
Katibu Mkuu wa CCM, Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro, amekutana na Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kiarabu ya Sahara (SADR), Mhe. Brahim Ghali. Katika mazungumzo hayo, aliwasilisha salaam za Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mazungumzo hayo yalifanyika tarehe 9 Aprili 2026 katika makazi rasmi ya Mhe. Ghali, Kambi ya Ausserd, Tindouf, Algeria. Balozi Migiro alisisitiza kuwa msimamo wa Tanzania na CCM wa kuunga mkono haki ya watu wa Saharawi kujitawala ni wa muda mrefu. Alieleza kuwa msingi wake uliwekwa tangu enzi za Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.

Kwa upande wake, Mhe. Ghali alimshukuru Rais Dkt. Samia kwa salaam na kwa kutuma uwakilishi kwenye maadhimisho ya miaka 50 ya SADR yaliyofanyika tarehe 8 Aprili 2026 katika Kambi ya Ausserd. Pia aliomba salamu zake zifikishwe kwa Rais, CCM na Watanzania.

Aliongeza kuwa watu wa Saharawi wanathamini mchango wa Mwalimu Nyerere katika kuhamasisha mshikamano wa Afrika na dunia. Alisema mshikamano huo umeendelea kuimarisha harakati za SADR, chini ya uongozi wa Chama cha Polisario, katika kudai haki ya kujitawala.





NA EMMANUEL MBATILO, MICHUZI TV

Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, amesema Serikali itaendelea kuweka mazingira rafiki kwa wanawake wajasiriamali kwa kuwaondolea vikwazo na kurahisisha taratibu za urasimishaji wa biashara ili waweze kushiriki kikamilifu katika uchumi wa taifa.

Dkt. Kapinga ameyasema hayo leo Aprili 12, 2026 Jijini Dar es Salaam wakati akizungumza katika Maadhimisho ya Women In Balance Kitchen Party Gala 2026, akieleza kufurahishwa kwake kushiriki kwa mara ya kwanza katika jukwaa hilo linalowaunganisha wanawake wajasiriamali kutoka ngazi mbalimbali.

Amebainisha kuwa jukwaa hilo limekuwa na mchango mkubwa kwa zaidi ya miaka 16 kwa kuwaunganisha wanawake wenye mitaji midogo, ya kati na hata wanaojihusisha na biashara za ndani na nje ya nchi, hali inayochochea maendeleo yao kijamii na kiuchumi.

“Jukwaa hili ni muhimu sana kwa maendeleo ya wanawake kijamii na kiuchumi. Limekuwa mstari wa mbele katika kuwaunganisha na kuwawezesha wanawake kuinuana,” amesema Waziri Kapinga.

Akizungumzia changamoto zinazowakabili wanawake, Waziri Kapinga amesema bado wapo wanaohofia kurasimisha biashara zao kutokana na mtazamo wa ugumu wa taratibu. Hata hivyo, alisisitiza kuwa Serikali imebadili mwelekeo na sasa inalenga kuwawezesha wafanyabiashara badala ya kuwaadhibu.

“Zama za kufungia biashara zimekwisha. Tukimkuta mama anafanya biashara bila leseni, tutamwelekeza na kumsaidia kupata vibali vinavyohitajika. Lengo letu ni kuwawezesha, si kuwaadhibu,” amesisitiza.

Aidha, ameeleza kuwa Serikali inaendelea kuboresha utoaji wa huduma kwa kusogeza karibu taasisi zinazohusika na biashara, hatua inayolenga kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wafanyabiashara, hususan wanawake na vijana.

Katika hatua nyingine, Waziri Kapinga amewahimiza wanawake kuchangamkia fursa zilizopo katika sekta ya viwanda vidogo, vya kati na vikubwa, akisisitiza kuwa wao ni sehemu muhimu ya utekelezaji wa maono ya taifa ya kujenga uchumi imara.

Ameongeza kuwa sekta binafsi ina mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi, huku akiwahamasisha wanawake kuwa mstari wa mbele katika biashara na uwekezaji.

“Wanawake ni jeshi kubwa. Tukiamua, tunaweza. Mafanikio ya mwanamke yako mikononi mwake kupitia ushirikiano na kujituma,” amesema.

Aidha, amepongeza waandaaji wa jukwaa hilo kwa kuendelea kuwa chachu ya kuwawezesha wanawake kiuchumi na kijamii, na kuahidi kuwa Serikali itaendelea kushirikiana nao katika juhudi za kuinua wanawake.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Women In Balance Kitchen Party Gala 2026Vida Nasari, amesema washiriki 200 walihudhuria tukio hilo na wengi wao ni wanawake wenye ushawishi katika jamii.

Amesema washiriki hao wako tayari kushirikiana na taasisi zilizo chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara, ikiwemo BRELASIDOTANTRADECBETBS na FCC, ili kupata elimu na taarifa sahihi zitakazowawezesha kusonga mbele.

Amesisitiza kuwa ushirikiano huo utakuwa mwanzo wa safari ya kuwajengea wanawake uwezo zaidi kiuchumi na kijamii.















Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita akikata keki na kuzindua kikundi cha Wanawake Chuma katika Tamasha la Mwanamke Chuma Msimu wa Tano -Picha - Malunde


Na Kadama Malunde, Malunde 1 Blog


Mamía ya wanawake wamejitokeza kushiriki Tamasha la Mwanamke Chuma Msimu wa Tano lililofanyika Aprili 11, 2026 katika Ukumbi wa Malex uliopo Kahama, mkoani Shinyanga, huku wito ukitolewa kwa wanawake kushirikiana na kuinua wenzao ili kufikia mafanikio ya pamoja.


Mgeni rasmi katika tamasha hilo alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita, aliyesisitiza umuhimu wa mshikamano, uthubutu na kujiamini kwa wanawake katika harakati za maendeleo binafsi na ya jamii.


Akizungumza katika tamasha hilo, Mhita amewataka wanawake kuacha hofu ya maneno ya watu na badala yake kuzingatia malengo yao kwa vitendo.


“Mwanamke hakikisha unapambana ili kufikia malengo yako, usiogope kusemwa. Wewe songa mbele kwa sababu uwe mzuri utasemwa, uwe mbaya utasemwa, upendeze utasemwa, usipendeze utasemwa. Kuna watu wamevunjika moyo kwa sababu ya kusemwa, hakikisha kuwa upo na watu sahihi, jiamini, usihangaike na watu wenye kukutisha tamaa. Ili mwanamke uonekane umefanikiwa, lazima uinue wanawake wenzako. Uwe nguzo ya kuwainua wengine,” amesema Mhita.

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita.


Akifafanua zaidi, Mhita amebainisha kuwa katika dunia ya sasa, mafanikio ya mwanamke yanategemea zaidi uthubutu wa kiuchumi, akisisitiza kuwa, “siri ya mwanamke yoyote ni sasampa (pesa), na habari ya mjini ni pesa, hivyo ni lazima mwanamke uhakikishe unazitafuta na kuzitumia fursa zinazokuwezesha kuinuka kiuchumi.”


Ameongeza kuwa wanawake wanapaswa kujiamini na kutumia kikamilifu fursa zilizowekwa na serikali, ikiwemo mikopo na uwezeshaji katika sekta mbalimbali kama madini, kilimo na viwanda, akibainisha kuwa mazingira rafiki yameboreshwa chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.


Amesema kuwa kupitia maboresho hayo, wanawake wachimbaji wa madini sasa wanapata mikopo na kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji, huku sekta ya kilimo ikipewa kipaumbele kwa kuongeza bajeti ili wanawake wanufaike zaidi.


Aidha, ameeleza kuwa hata katika sekta ya viwanda wanawake wameendelea kunufaika na fursa zilizopo na kuchangia ukuaji wa uchumi.

Mhita amewapongeza wanawake wa Ushetu kwa jitihada zao katika kusindika na kuongeza thamani ya mazao, akieleza kuwa huo ni mfano bora wa namna wanawake wanavyoweza kutumia fursa za kiuchumi kujiletea maendeleo endelevu.


Pia amegusia mafanikio yaliyopatikana katika sekta ya afya na elimu, akieleza kuwa Serikali imeendelea kuboresha huduma za afya kwa wananchi, huku Mkoa wa Shinyanga ukiwa sasa na shule sita za wasichana, hatua inayochochea upatikanaji wa elimu kwa mtoto wa kike na kumjengea msingi imara wa mafanikio ya baadaye.


Akisoma risala kwa mgeni rasmi, Mkurugenzi wa Gold FM na mwandaaji wa tamasha hilo, Bi. Neema Mghen, amesema Tamasha la Mwanamke Chuma limeendelea kuwa zaidi ya tukio la kawaida na sasa ni jukwaa muhimu la mabadiliko kwa wanawake.

Neema Mghen


Amesema kupitia tamasha hilo, wanawake wengi wamefanikiwa kujikwamua kiuchumi, kujitambua, kujiamini na kushiriki kikamilifu katika nafasi za uongozi na maamuzi ndani ya familia na jamii.


Kaulimbiu ya mwaka huu, “Nguvu ya Ujasiri,” imelenga kuhamasisha wanawake kusimama bila uoga, kuchukua hatua na kutumia fursa zilizopo kubadilisha maisha yao na ya wengine.


Ametaja mafanikio ya msimu wa tano kuwa ni pamoja na kuanzishwa kwa kikundi cha Mwanamke Chuma Maendeleo Group kilichozinduliwa rasmi wakati wa Tamasha la Mwanamke Chuma 2026, kusaidia wanawake wa gereza la Kahama kwa kuwapatia mahitaji muhimu, pamoja na kuendeleza utamaduni wa kutoa tuzo kwa wanawake ili kutambua na kuhamasisha juhudi zao.

Hata hivyo, amebainisha changamoto zinazowakabili wanawake kuwa ni pamoja na ukosefu wa mitaji na utaalamu katika sekta ya uchimbaji mdogo wa madini, uwepo wa mikopo yenye riba kubwa na masharti magumu, pamoja na changamoto za pembejeo bora na masoko ya uhakika katika sekta ya kilimo.


“Tunaamini ukimuinua mwanamke, umeinua familia na jamii kwa ujumla. Ujasiri wa mwanamke si kelele bali ni hatua, si maneno bali ni matendo,” amesema Mghen.


Ameongeza kuwa Tamasha la Mwanamke Chuma lina lengo la kukuza uchumi wa wanawake mmoja mmoja na vikundi, kujenga mshikamano, uthubutu na kuimarisha sauti ya pamoja ya wanawake katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi.


Katika tamasha hilo lililoandaliwa na Kituo cha Redio cha Gold FM, viongozi mbalimbali wamehudhuria akiwemo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga SACP Janeth Magomi, Mbunge wa Ushetu Mhe. Emmanuel Cherehani na Mbunge wa Kahama Mjini Mhe. Benjamini Ngayiwa, pamoja na wadau mbalimbali wa maendeleo.
Tamasha hilo limepambwa na burudani kutoka kwa msanii mkongwe wa muziki wa taarab, Mzee Yusuph, huku uendeshaji wa shughuli ukifanywa na MC maarufu Dkt. Kumbuka na mtaalamu wa maendeleo ya familia na uchumi, Dkt. Chris Mauki, aliyetoa mada mbalimbali zilizolenga kuwainua wanawake kiuchumi na kijamii.


Aidha, jumla ya tuzo tisa za ushindani zimetolewa kwa washindi waliopatikana kupitia kura za wananchi, pamoja na tuzo maalum za heshima na vyeti kwa wadau waliotoa mchango mkubwa katika kuwawezesha wanawake.


Tuzo hizo zimetolewa kwa wanawake waliobobea katika nyanja mbalimbali zikiwemo ujasiriamali, madini, ubunifu, ushonaji, upishi, saluni pamoja na wanawake wenye ushawishi chanya katika jamii, hatua inayolenga kuhamasisha wanawake wengine kujituma na kufikia mafanikio.


ANGALIA MATUKIO KATIKA PICHA

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita akizungumza kwenye Tamasha la Mwanamke Chuma Msimu wa Tano lililofanyika Aprili 11, 2026 katika Ukumbi wa Malex uliopo Kahama, mkoani Shinyanga - Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog


Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita akizungumza kwenye Tamasha la Mwanamke Chuma Msimu wa Tano lililofanyika Aprili 11, 2026 katika Ukumbi wa Malex uliopo Kahama, mkoani Shinyanga

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita akizungumza kwenye Tamasha la Mwanamke Chuma Msimu wa Tano lililofanyika Aprili 11, 2026

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita akiimba na kucheza na Wanawake Chuma kwenye Tamasha la Mwanamke Chuma Msimu wa Tano

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita akizindua kikundi cha Wanawake Chuma katika Tamasha la Mwanamke Chuma Msimu wa Tano

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita akikabidhi katiba ya kikundi cha Wanawake Chuma katika Tamasha la Mwanamke Chuma Msimu wa Tano

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita akikata keki katika Tamasha la Mwanamke Chuma Msimu wa Tano

Mwandaaji wa Tamasha la Mwanamke Chuma 2026 ambaye pia ni Mkurugenzi wa Kituo cha Redio cha Gold FM, Bi. Neema Mghen akisoma risala kuhusu Tamasha la Mwanamke Chuma

Mwandaaji wa Tamasha la Mwanamke Chuma 2026 ambaye pia ni Mkurugenzi wa Kituo cha Redio cha Gold FM, Bi. Neema Mghen akisoma risala kuhusu Tamasha la Mwanamke Chuma

Mbunge wa Jimbo la Ushetu Mhe. Emmanuel Cherehani akizungumza katika Tamasha la Mwanamke Chuma 2026

Mbunge wa Jimbo la Kahama Mjini Mhe. Benjamini Ngayiwa akizungumza katika Tamasha la Mwanamke Chuma 2026

Mwandaaji wa Tamasha la Mwanamke Chuma 2026 ambaye pia ni Mkurugenzi wa Kituo cha Redio cha Gold FM, Bi. Neema Mghen akikabidhi tuzo ya Heshima kwa Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Mboni Mhita. Kushoto ni Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga SACP Janeth Magomi

Mtaalamu wa maendeleo ya familia na uchumi, Dkt. Chris Mauki akitoa mada kwenye tamasha la Mwanamke Chuma 2026

Mtaalamu wa maendeleo ya familia na uchumi, Dkt. Chris Mauki akitoa mada kwenye tamasha la Mwanamke Chuma 2026





Msanii Mkongwe wa Taarabu, Mzee Yusuph akitoa Burudani

Msanii Mkongwe wa Taarabu, Mzee Yusuph akitoa Burudani










































TAZAMA PICHA ZAIDI HAPA - TAMASHA LA MWANAMKE CHUMA 2026


Top News