Na Pamela Mollel,Longido

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mwigulu Nchemba, amepongeza maendeleo ya ujenzi wa Mradi wa Majisafi wa Sinya–Namanga, akieleza kuwa utekelezaji wake ni hatua muhimu katika kumaliza tatizo la maji lililodumu kwa miaka mingi katika maeneo hayo.

Dkt. Nchemba alikagua mradi huo Februari 23, 2026 katika eneo la Sinya, wilayani Longido mkoani Arusha na kujionea maendeleo ya kazi yanayoendelea. Alisema kukamilika kwa mradi huo kutaleta mabadiliko makubwa kwa wakazi wa Sinya na Namanga, hasa katika kuboresha huduma za kijamii na shughuli za kiuchumi.

Mradi huo unatarajiwa kuzalisha lita milioni 4.1 za maji safi kwa siku, kiwango kitakachoongeza upatikanaji wa maji kwa matumizi ya majumbani, taasisi za kijamii pamoja na mifugo. Eneo hilo limekuwa likikabiliwa na changamoto ya uhaba wa maji kutokana na kuongezeka kwa mahitaji, huku chanzo cha Mto Simba kikishindwa kukidhi mahitaji yaliyopo.

Utekelezaji wa mradi unasimamiwa na mkandarasi Zongii Contractors Co. LTD kwa gharama ya shilingi bilioni 13.5, fedha zinazotolewa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kwa mujibu wa taarifa ya utekelezaji, hadi Januari 2026 mradi ulikuwa umefikia asilimia 24.7 ya utekelezaji, huku hatua mbalimbali za awali zikiendelea kukamilishwa.

Akizungumza na wananchi, Waziri Mkuu anasema serikali imejipanga kuhakikisha miradi ya maji inatekelezwa kwa wakati na kwa viwango vinavyokidhi ubora unaotakiwa, ili kuondoa adha ya wananchi kutembea umbali mrefu kutafuta maji. Aliongeza kuwa upatikanaji wa maji wa uhakika utachochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika ukanda huo wa mpakani.





Tume ya Ushindani (FCC) imesema itaendelea na mchakato wa marekebisho ya sheria zake kwa lengo la kuimarisha ulinzi wa walaji, kudhibiti bidhaa bandia na kuhakikisha kunakuwepo ushindani wa haki unaochochea ukuaji wa uchumi na ajira nchini.


Hayo yamesemwa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Khadija Ngasongwa, wakati akifungua semina ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari iliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Ngasongwa amesema marekebisho hayo yanalenga kumlinda mlaji dhidi ya bidhaa zisizo na ubora, matangazo ya upotoshaji pamoja na vitendo vinavyokwenda kinyume na misingi ya ushindani wa haki sokoni.

Amesema moja ya vipaumbele vya Tume hiyo ni kuimarisha udhibiti wa bidhaa bandia zinazoingia sokoni, akibainisha kuwa bidhaa hizo huathiri afya za wananchi, hupunguza mapato ya Serikali na kuwanyima wafanyabiashara halali fursa ya kukuza biashara zao.

“Jukumu letu ni kuhakikisha uchumi unakua kwa misingi ya ushindani wa haki. Matokeo yake ni kuongezeka kwa uwekezaji na ajira kwa wananchi,” alisema Ngasongwa.

Aidha, amesema FCC itaendelea kukutana mara kwa mara na waandishi wa habari pamoja na wadau mbalimbali kwa lengo la kutoa taarifa sahihi kuhusu majukumu yake na kusikiliza changamoto za wananchi ili kuzipatia ufumbuzi kwa wakati.

Katika hatua nyingine, amesema kuna maboresho yanayofanyika kupitia TANOGA — muunganiko wa taasisi za Serikali za udhibiti pamoja na mawakala wa forodha — kwa lengo la kuimarisha usimamizi wa bidhaa zinazoingia nchini.

Ngasongwa ameongeza kuwa taasisi hizo zinaelekea kuingia katika mfumo wa kidijitali utakaopunguza mwingiliano wa moja kwa moja kati ya watumishi na wateja, hatua itakayosaidia kuongeza uwazi, kupunguza urasimu na kudhibiti mianya ya vitendo visivyo vya kiadilifu.

FCC imeahidi kuendelea kushirikiana na taasisi nyingine za Serikali pamoja na sekta binafsi ili kuhakikisha mazingira ya biashara nchini yanabaki kuwa salama, yenye ushindani wa haki na yenye manufaa kwa wananchi.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), Khadija Ngasongwa, akizungumza wakati akifungua semina ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari iliyoandaliwa na Tume hiyo, iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana, Februari 24, 2026.
Makamu wa Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi Habari Mkoa wa Dar ea Salaam (DARPC) Mary Geofrey akitoa maelezo kuhusiana na semina ya FCC itavyochochea ushindani wa soko ,jijini Dar es Salaam.
Semanina ikiendelea 
Picha pamoja ya wafanyakazi wa FCC na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC Khadija Ngasongwa katika Semina ya Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam.
Picha pamoja ya waandishi wa Habari na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC Khadija Ngasongwa katika Semina ya Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam.









Kwa masikitiko makubwa na huzuni nzito, tumepokea taarifa ya kifo cha Mwadhama Polycarp Cardinali Pengo, Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam.

Marehemu alikuwa mchungaji mwaminifu na kiongozi mwenye hekima na busara, aliyeilitumikia Kanisa na Taifa kwa uaminifu mkubwa, akiacha alama isiyofutika katika mioyo ya wengi.

Kwa niaba yangu binafsi na kwa niaba ya Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO), ninawasilisha salamu za rambirambi kwa Kanisa Katoliki, familia ya marehemu, waumini wote, na Watanzania wote walioguswa na msiba huu mkubwa katika Kanisa na Taifa letu.

Tunamwomba Mwenyezi Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi, apumzike kwa amani ya milele.

“Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo alikuwa kama sisi, nasi tutakuwa kama yeye; hivyo tujiandae.”

Imetolewa na:
Boniventura Mwalongo
Katibu Mkuu – TRAMEPRO

Tarehe: 24 Februari 2026





 

Meneja wa Ukaguzi wa Sekta za Umma, kutokea Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Bi. Rosemary Ruganuza,amezitaka taasisi za sekta ya umma kutumia kwa usahihi Mfumo Jumuishi wa Usimamizi wa Kodi za Ndani (IDRAS) ili kuongeza uwazi, uwajibikaji na ufanisi katika ukusanyaji na usimamizi wa mapato ya Serikali.

Kauli hiyo ameitoa leo Februari 25 Jijini Dodoma wakati akifungua mafunzo ya mfumo wa IDRAS yaliyoandaliwa na Idara ya Walipakodi Wakubwa wa TRA kwa taasisi za umma.

Bi. Ruganuza amesema matumizi sahihi ya mfumo huo yatasaidia taasisi za umma kutekeleza majukumu yao ya kikodi kwa wakati, kwa usahihi na kwa kuzingatia sheria na kanuni za kodi.

Amesema IDRAS ni sehemu ya mageuzi ya kidijitali yanayolenga kurahisisha huduma za kikodi, kupunguza makosa ya kibinadamu na kuongeza ufuatiliaji wa taarifa za walipakodi kwa njia ya kielektroniki.

“Matumizi sahihi ya IDRAS yataimarisha uwajibikaji, kuongeza uwazi na kuhakikisha majukumu ya kikodi yanatekelezwa kwa wakati na kwa usahihi. Ni wajibu kwa kila taasisi kuwa balozi wa ndani ya eneo lake la kazi,” asema Bi. Ruganuza.


WANANCHI wa Kata ya Mzenga na Mafizi wamepongeza hatua ya Mbunge wao, Dkt. Selemani Jafo, kusimamia binafsi ujenzi wa Daraja la Kitomondo hadi usiku, wakisema imeongeza kasi na uwajibikaji kwa mkandarasi.

Akizungumza kwa niaba ya wananchi wa Mafizi, mmoja wa wazee wa eneo hilo, Ramadhani Zungwe amesema si jambo la kawaida kwa kiongozi kubaki kijijini hadi usiku akihakikisha kazi inafanyika kama ilivyopangwa.

“Ameonyesha mfano wa kujitoa kwa ajili ya maendeleo yetu. Hii inatupa matumaini mapya,” amesisitiza Zungwe.

Msukumo huo umefuatia maelekezo aliyoyatoa Dkt. Jafo wiki iliyopita kwa mkandarasi, kampuni ya Neloyt Tanzania Limited, akitaka ifikapo tarehe 24 nguzo za daraja hilo ziwe tayari zimemwagwa.

Tangu wakati huo, kazi imekuwa ikiendelea kwa kasi kubwa, huku Dkt. Jafo mwenyewe akishuhudia hatua za ujenzi zinavyopiga hatua.

Naye, Diwani wa Kata ya Mafizi, Mhe. Bora Mayage, amekiri kuwa usimamizi wa karibu wa mbunge huyo umeleta matokeo chanya.

Amesema kasi ya awali ya mkandarasi haikuwa ya kuridhisha, lakini kwa sasa mabadiliko yanaonekana wazi na nguzo za zege tayari zimesimama.

Mbali na hayo, Dkt. Jafo amemtaka mkandarasi kuhakikisha ifikapo Machi 5 zoezi la umwagaji wa slab linakamilika, akiahidi kushiriki pamoja na viongozi wa kata hizo mbili katika hatua hiyo muhimu.

Ameweka bayana kuwa hatokuwa tayari kuona wananchi wake wanaendelea kuteseka wakati Rais, Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan ameshatoa pesa ya kukamilisha daraja hilo.

Daraja la Kitomondo linatajwa kuwa kiungo muhimu kwa wakazi wa Mzenga na Mafizi, likirahisisha shughuli za kijamii na kiuchumi zikiwemo usafiri wa wanafunzi, wafanyabiashara na wagonjwa.

Kukamilika kwake kunatarajiwa kufungua ukurasa mpya wa maendeleo kwa wananchi wa maeneo hayo.

Na Munir Shemweta, WANMM

Serikali kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeyapatia ufumbuzi malalamiko ya muda mrefu ya viwanja mbadala kwa wananchi wa jiji la Dodoma.

Suluhisho hilo linafuatia malalamiko ya takriban wananchi 4000 wa jiji la Dodoma wanaodai viwanja na halmashauri ya jiji la Dodoma kuwapa ahadi bila kutekeleza mpaka sasa.

Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 25 Februari 2026 na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo wakati akizungumza na wananchi wenye migogoro ya ardhi katika eneo la Mahomanyika lilopo kata ya Nzuguni jijini Dodoma.

Dkt Akwilapo amesema, eneo la Mahomanyika ni eneo la serikali hivyo lipangwe na kupimwa kwa ajili ya utatuzi wa migogoro ya meneo mbalimbali ya jiji la Dodoma pamoja na matumizi ya serikali.

"Eneo hili lenye mgogoro hapa Mahomanyika ni eneo la serikali hivyo lipangwe na kupimwa kwa ajili ya utatuzi wa migogoro na siyo ya hapa tu na mingine ya jiji la Dodoma na matumizi ya serikali" amesema.

Amesisitiza kuwa katika upangaji wa eneo hilo kipaumbele kiwe kutatua changamoto za wananchi wa jiji la Dodoma ambao kwa muda mrefu wamedai viwanja na jiji kuwaahidi bila ya kuwapatia.

Katika kufanikisha zoezi hilo, zimeundwa timu mbili kwa ajili ya upangaji na upimaji na pamoja na ile ya kushughulika na uhakiki wa wananchi wenye migogoro na kustahili kupatiwa viwanja mbadala.

"Timu hizi zitaanza kazi mara moja na kazi hiyo itafanyika kwa muda wa siku sitini, miezi miwili kazi iwe imekamilika kila mtu kujua amepata nini na anaenda wapi" amesema.

Akigeukia uuzwaji viwanja 1,037 vilivyoingizwa kwenye mfumo wa TAUSI ili wananchi wapate viwanja vilivyopimwa katika eneo la Mahomanyika, Dkt. Akwilapo amuagiza Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma kuendelea na uuzaji viwanja kwa waombaji 352 pekee walioanza kulipa huku wale ambao hawajaanza kulipa maombi yao yasitishwe.

Eneo la Mahomanyika limekuwa na changamoto ya malalamiko ya muda mrefu kutoka kwa wananchi wakidai ni wamiliki wa asili wa maeneo hayo jambo lililosababisha kuundwa kwa Timu (Timu ya DC) ambayo ilishirikisha wananchi, Vyombo vya Usalama na Wataalam ambapo timu hiyo ilibaini eneo husika ni eneo la Serikali.
 Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe, Dkt Leonard Akwilapo akizungumza na wananchi wa eneo la Mahomanyika katika kata ya Nzuguni alipokwenda kutoa tamko la serikali kuhusiana na mgogoro wa ardhi kwenye eneo hilo tarehe 25 Februari 2026.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemery Senyamule akizungumza wakati wa mkutano wa Waziri wa Ardhi na wananchi wa eneo la Mahomanyika jijini Dodoma tarehe 25 Februari 2026.




Sehemu ya wananchi wa eneo la Mahomanyika katika kata ya Nzuguni jijini Dodoma wakimsikiliza Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Leonard Akwilapo (Hayupo pichani) alipokwenda kuzungumza nao kuhusiana na mgogoro wa ardhi katika eneo hilo.
Mkuu wa wilaya ya Dodoma Jabir Shekimweri akizungumza wakati wa mkutano na wananchi wa eneo la Mahomanyika jijini Dodoma tarehe 25 Februari 2026. (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)

Katika tukio la kipekee kabisa kwenye kipindi hiki cha mfungo wa Ramadan na Kwaresma limegusa watu wengi katika kusheherekea kwa pamoja na familia zao kwa chakula kinacho andaliwa na wataalam na wabobezi wikiendi hii ya tarehe 28 February na 1 March 2026 MBEZI BEACH RAINBOW Dar es salaam.

Lavender Catering itaandaa menu ya kifahari yenye vionjo mbalimbali ambavyo baadhi ni kama vile Fish Samosas, Bagia laini, Kalmati, Cream of Vegetable Soup na Uji moto kwa kuanzia.

Chakula kikuu kitakua na mchanganyiko wa ladha mbalimbali: Saffron Rice, Samaki Masala, Orange Chicken, Crispy Beef, Mzuzu wa Nazi na Iliiki, Chips Masala, Sweet Raisins Noodles ,Chicken Liver na kadhaliika.

Kwa kumalizia, wageni watapata Mango Mousse laini, Banana Nutella Pancakes, na matunda fresh, pamoja na vinywaji kama Karak Chai, Kahawa, Maji, na Fresh Juice.

Kwa Watu wazima watalipa TSH 30,000 kwa chakula, wakati watoto wenye umri wa miaka 4–10 watalipa TSH 18,000 tu. Mazingira ya ufukweni yakipamba kufturi kuwe kwa kukumbukwa, kwa chakula kitamu na furaha ya pamoja.

Tukio hili sio la kukosa watu wa dini zote watahudhiria na kufanya mfungo huu kwa kipekee. Kwa maelezo zaidi wasliana na Chief +255 788 500 067.



Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imesema jumla ya malalamiko 549
(Administrative Reviews) yamewasilishwa na kushughulikiwa na Taasisi Nunuzi kupitia Moduli jambo linaloonyesha mwitikio chanya kutoka kwa wazabuni na Taasisi Nunuzi katika kutumia mfumo kwa ajili ya kupokea, kuchambua na kutoa maamuzi kuhusu malalamiko yanayohusu michakato ya ununuzi wa Umma.

Jumla ya rufaa 26 zimewasilishwa na kushughulikiwa na Mamlaka ya Rufani kupitia moduli hiyo, hatua ambayo imeongeza ufanisi katika usimamizi wa rufaa, kupunguza muda wa kushughulikia mashauri, na kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika utoaji wa haki.

James Sando Katibu Mtendaji Mamlaka ya Rufani ya Wazabuni za Umma (PPAA) ameyabainisha hayo leo jijini Dodoma katika Makutano na Waandishi wa Habari akitangaza miradi ya maendeleo na fursa za vijana kwa mwaka 2025/20.

Sando amesema kwa ujumla, takwimu hizo zinaonesha mafanikio makubwa ya awali katika matumizi ya Moduli ya kushugulikia Malalamiko na Rufaa, zinaimarisha mifumo ya ununuzi wa umma nchini kwa kuhakikisha uwazi, uwajibikaji na ufanisi katika mchakato wa Ununuzi.

Katika kuendeleza azma ya Serikali ya kuimarisha uwazi, uwajibikaji, na ufanisi katika sekta ya ununuzi wa umma hususan ushughulikiwaji wa malalamiko na rufaa zinazotokana na michakato ya ununuzi wa umma,

Mamlaka ya Rufani kwa kushirikiana na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), imekamilisha ujenzi wa Moduli ya Kupokea na kushughulikia Malalamiko na Rufaa zinazotokana na michakato ya Ununuzi wa Umma (Complaints and Appeals Management Module).

"Moduli hii ipo katika Mfumo wa Ununuzi wa Umma kwa Njia ya Kielektroniki (NeST), na inatoa njia rahisi, ya haraka, na yenye uwazi kwa wadau wote kushiriki katika mchakato wa usulushi wa migogoro ya ununuzi"

Amesema inachangia kwa kiasi kikubwa kuboresha utendaji na kuimarisha imani katika mfumo wa ununuzi wa umma.

Hata hivyo Sando amesema Serikali kupitia Wizara ya Fedha ilizindua rasmi matumizi ya moduli hiyo Februari 2025, Tangu uzinduzi huo, moduli imeleta mageuzi chanya katika namna taasisi za umma zinavyoshirikiana na Mamlaka ya Rufani kupokea, kusajili na kushughulikia malalamiko na rufaa kutoka kwa wazabuni walioshiriki katika michakato ya ununuzi wa umma na kwa sasa, malalamiko yote yanawasilishwa kupitia moduli ya Usimamizi wa Malalamiko na Rufaa katika mfumo wa NeST.

"Moduli hii imeendelea kutumika na wadau mbalimbali kwa madhumuni ya kuwasilisha na kushughulikia malalamiko na rufaa kwa njia ya kielektroniki, ikileta ufanisi mkubwa katika mchakato mzima.

Sando atoa wito kwa wazabuni wote nchini pamoja na wadau wa ununuzi wa umma kushiriki mafunzo ya matumizi ya moduli hiyo pale Mamlaka ya Rufani inapoyatangaza Mafunzo.

yatawawezesha kuelewa namna bora ya kutumia moduli hiyo pale wanapokabiliwa na changamoto katika michakato ya ununuzi wa umma.




Na Pamela Mollel, Arusha

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mwigulu Nchemba, ameonyesha kuridhishwa na mwenendo wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayoendelea katika Jiji la Arusha, akisema kasi iliyopo inaleta matumaini mapya kwa wananchi.

Katika ziara yake ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa stendi kuu ya mabasi katika eneo la Bondeni City,Waziri Mkuu alisisitiza umuhimu wa miundombinu bora itakayokidhi mahitaji ya ukuaji wa jiji hilo. Alielekeza pia ujenzi wa barabara za njia nne ili kupunguza msongamano wa magari, sambamba na kuhimiza matumizi ya mabasi ya mwendokasi yanayotumia nishati safi ikiwemo gesi na umeme.

Akizungumza na wananchi na viongozi wa eneo hilo, Dkt. Nchemba alisema utekelezaji wa miradi hiyo ni sehemu ya dhamira ya Serikali katika kuimarisha huduma za kijamii na kukuza uchumi wa taifa. 

Alibainisha mafanikio yaliyopatikana katika sekta mbalimbali zikiwemo afya, elimu na nishati, akitolea mfano ujenzi wa hospitali za wilaya, vituo vya afya na zahanati pamoja na upatikanaji wa vifaa tiba vya kisasa katika hospitali za rufaa na mikoa.

Aidha, aliwataka wakandarasi waliolipwa na Serikali kuhakikisha wanalipa wafanyakazi wao kwa wakati, akionya kuwa haki za wafanyakazi zinapaswa kulindwa. Kuhusu vizimba vya wafanyabiashara katika stendi hiyo, alisisitiza vitolewe kwa walengwa halisi wanaofanya biashara badala ya kuhodhiwa kwa lengo la kupangisha kwa bei ya juu.

Katika ziara hiyo, Waziri Mkuu alipokea na kutatua baadhi ya kero za wananchi, akiahidi kuendeleza utaratibu huo katika maeneo mengine nchini.

Kwa upande wake, Waziri wa Habari, Michezo, Sanaa na Utamaduni, Paul Makonda, alimpongeza Waziri Mkuu kwa msisitizo wake wa kusikiliza changamoto za wananchi na kuzitafutia suluhisho. Alieleza kuwa Arusha kuna jumla ya miradi 52 inayoendelea kutekelezwa kwa kuzingatia Ilani ya Chama Cha Mapinduzi.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Amos Makalla, aliwahimiza wakandarasi kuongeza bidii ili kuhakikisha miradi inakamilika kwa wakati. Aliahidi ushirikiano wa karibu kati ya ofisi yake na wadau mbalimbali ili kusimamia utekelezaji wa miradi hiyo.

Hata hivyo, alionya dhidi ya migogoro isiyo ya lazima kati ya wafanyabiashara na baadhi ya watumishi wasio waadilifu, akisisitiza umuhimu wa uwajibikaji na maadili katika utekelezaji wa majukumu ya umma.





Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe Adolph Mkenda afungua mlango wa mazungumzo kwa Taasisi na Makampuni mbalimbali kuunga mkono juhudi za Rais Dkt Samia kusomesha Wanafunzi wanaofanya vizuri katika masomo ya Sayansi kutoka ngazi ya awali ya kidato cha sita hadi ngazi ya Shahada ya Uzamili kwani Wizara imejipanga vizuri kuhakikisha fedha watakazotoa zinakwenda mahali panapotakiwa

Waziri Mkenda ameyasema hayo leo Jijini Dodoma Februari 25,2026 wakati akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu kutolewa kwa ufadhili huo na Wanafunzi kuripoti katika Vyuo husika.

Ambapo amesema kuwa tayari walishapanga kutoa ufadhili katika ngazi ya Shahada ya Uzamili na kwa kuanza waliamua kupeleka Wanafunzi katika Vyuo viwili vya hapa nchini cha Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Arusha na kampasi ya Indian Institute of Teknoloji kilichopo Zanzibar ambavyo vyote vimejikita katika masuala ya Sayansi. 

Na kuongeza kuwa tayari Wanafunzi wamesharipoti katika Chuo cha Nelson Mandela na kuanza masomo kwa ngazi ya Shahada ya Uzamili na kwa awamu ya pili watawapeleka wengine tena 10 katika kampasi ya Indian Institute of Teknoloji kwaajili ya kusoma  mambo ya Data Science,Akili unde na mambo mengine ya kisayansi ili kuendana na kasi ya Dunia katika Sayansi na Teknolojia. 

"Kwahiyo napenda nitoe kauli hii kwa Benki,Migodi,Taasisi na Mashirika mbalimbali ambayo yanapenda kuunga mkono juhudi za Rais wetu za kusomesha tukae tuongee na tutakuwa na mkutano wa kuzungumza pamoja na kuwahakikishia tutakavyogawa nafasi bila bila kona kona ili hela mtakazoleta ziende mahali panapotakiwa".

Aidha amesema kuwa kwa mwaka huu wameanza kutekeleza maelekezo ya Serikali kwa kupeleka vijana waliofanya vizuri kwenda kusoma masuala ya Data Science, Akili unde na mambo mengine ya kisayansi ambapo tayari wameshapeleka wanafunzi 16 huko Johannesburg Afrika ya Kusini na wameanza masomo kwa ufadhili huo.

Ambapo pia wanafunzi wengine 34 wanatajiwa kuondoka kati ya mwezi wa 8 au 9 kwenda Iland kwaajili ya masomo hayo hayo ya Sayansi. 

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu Tume ya Sayansi na Teknolojia ambao ndio waratibu wa Program hiyo ya Samia Scholarship Extended Dkt Amos Nungu amesema kuwa wameona muitikio mkubwa kwa watoto na thamani ambayo watoto wameipa program hiyo,na kuamini kuwa idadi itaongezeka kwa wakati mwingine, zaidi ya hawa walioenda katika awamu hii.

Naye Makamu Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Arusha ambao ndio watekelezaji wa programu hii Prof Maulilio Kipanyula amesema Taasisi hiyo haikuchaguliwa kwa bahati mbaya kwasababu Wanafunzi wanaokwenda pale wanapata kuchanganyikana na wanafunzi kutoka Mataifa mengine kwani asilimia 10 ya wanafunzi wao ni wa Kimataifa hivyo wanapata uzoefu kupitia kukutana kwao na kuwa pamoja.






 


Top News