Na MASHAKA MHANDO, Tanga

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amepokea kwa majonzi makubwa kifo cha nguli wa muziki wa dansi nchini, Hayati Stephen Hiza (80), aliyetunga na kuimba wimbo wa kitaifa wa uzalendo, "Tanzania Nchi ya Furaha."

Hayati Mzee Hiza amehifadhiwa leo, Februari 18, 2026, katika nyumba yake ya milele eneo la Mwanzange, jijini Tanga. Akiwa na historia iliyotukuka, Mzee Hiza atakumbukwa kwa utunzi wake uliotikisa Radio Tanzania (RTD) mwaka 1967 akiwa na bendi kongwe ya Atomic Jazz ya Tanga, akizalisha vibao vilivyodumu vizazi na vizazi kama "Leo Nakupasulia", "Hamida Wangu", na "Sitamani Kitu".

Alama ya Mwaka 1967 na Uzalendo

Wimbo uliompa heshima ya kipekee na kumfanya atambulike kama "Mzalendo Namba Moja" wa sanaa ni "Tanzania Nchi ya Furaha". Wimbo huu, uliotungwa miaka sita tu baada ya Uhuru, umekuwa utambulisho wa amani na furaha ya Watanzania, jambo ambalo Rais Samia amesema litaacha alama isiyofutika.


Salamu za Pole na Tuzo ya Rais

Akizungumza kwa niaba ya Rais, Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma (MwanaFA), amesema Rais Dkt. Samia aliguswa na mchango wa Mzee Hiza kiasi cha kutoa zawadi ya Shilingi Milioni 50 pamoja na tuzo ya heshima kupitia Tanzania Music Awards (TMA) mwaka 2024.

"Mzee Hiza ni kielelezo cha wasanii waliotumia vipaji vyao kujenga taifa. Rais aliipokea kwa furaha ajenda ya kumtuza Mzee Hiza kwa sababu anaijua thamani ya kazi yake tangu enzi za Atomic Jazz," alisema MwanaFA.

MwanaFA na Ahadi ya Rekodi

MwanaFA amesimulia kwa masikitiko kuwa katika tamasha la 'Hale Festival' mwishoni mwa mwaka jana, Mzee Hiza alimweleza kuwa ana nyimbo mpya alizomtungia Rais na alikuwa na shauku ya kuzirekodi. "Niliahidi kumgharamia kurekodi kwa fedha zangu, lakini Mungu amempenda zaidi kabla ya kutekeleza dhamira hiyo," alisema Naibu Waziri huyo.

Rambirambi na Heshima za Mwisho

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dkt. Batilda Burian, amethibitisha kuwa Rais Samia ametuma rambirambi ya Shilingi Milioni 20 kupitia kwa Msaidizi wake wa Kijamii, Tido Mhando

Naye Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga na Mjumbe wa Kamati Kuu (MCC), Ustadh Rajab Abdalrahaman, pamoja na Meya wa Jiji la Tanga, Muhina Mustapha 'Seleboss', wameeleza kuwa pengo la Mzee Hiza halitazibika kwani alikuwa muumini wa muziki wa maadili na malezi kwa jamii.

Mzee Stephen Hiza amefariki akiwa na umri wa miaka 80, akiiacha Tanga na Tanzania katika simanzi, lakini akituachia urithi wa sauti yake ya dhahabu inayotuambia: "Tanzania, Tanzania, nchi yenye furaha...".















-Akagua ujenzi wa Chuo cha VETA Same.

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema kuwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ni Rais wa Matokeo na amedhihirisha hayo katika kipindi chake cha uongozi.

Amesema hayo leo Februari 18, 2026 alipokagua maendeleo ya ujenzi wa mradi wa Chuo cha VETA katika Wilaya ya Same, Tarafa ya Chome Suji Kata ya Makanya.

Ujenzi wa Chuo hicho utagharimu kiasi cha Shilingi Bilioni 1.4 kutoka Serikali kuu ili kukamilisha ujenzi wa Chuo hicho kwa awamu ya kwanza na mpaka sasa kiasi cha Shilingi milioni 542 kimeshapokelewa Wilayani hapo

Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amesema kuwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alipoingia madarakani kulikuwa na wilaya zaidi ya 60 ambazo hazikuwa na mradi wowote wa VETA lakini alielekeza wilaya zote ambazo hazina VETA zijengwe ikiwemo na mikoa isiyokuwa na vyuo hivyo”

“Lakini pia alikuta kuna Wilaya zaidi ya 119 hazina hospitali za Wilaya, pia alikuta zaidi ya kata 649 hazikuwa na vituo vya afya, ndani ya kipindi chake amejenga hospitali zote 119 za Wilaya pamoja na vituo 649 kwenye tarafa na kata za kimkakati”

Aidha, Dkt. Mwigulu amesema kuwa Rais Dkt. Samia amejenga zaidi ya shule za Sekondari 1300 ikiwemo shule maalum kwa Wasichana kwenye kila Mkoa “Pia amejenga shule za Msingi 2700 pamoja na kujenga madarasa 79,000 kwa ajili ya watoto wa Kitanzania”

Kuhusu ujenzi wa barabara ya Makanya - Chankonko - Mvungo yenye urefu wa km 33, amewaelekeza Halmashauri hiyo wafuate taratibu ili ihamishiwe Wakala wa Barabara (TANROADS) kwani ikibakia TARURA na kuendelea kujengwa kilomita moja au mbili haitamalizika. Barabara hiyo inapitisha magari makubwa yanayobeba mizigo ya jasi.

Akizungumza katika mkutano huo, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda amesema kuwa ujenzi wa chuo hicho utasaidia kuzalisha rasilimali watu itakayochagiza kuleta maendeleo katika Sekta sekta mbalimbali ikiwemo Viwanda.









Na Festo Polea

TUME ya Uchunguzi wa Matukio ya Uvunjifu wa Amani yaliyojitokeza wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, leo Februari 17, 2026 imekutana na Mwanasheria Andrew Chenge.

Mkutano huo wa Tume na Chenge umefanyika katika ukumbi wa Tanganyika uliopo jengo la Benki Kuu ya Tanzania (BoT) mkoani hapa, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Tume kukusanya taarifa, maoni na ushauri kutoka kwa viongozi mbalimbali.

Katika mkutano huo hoja zilizojadiliwa zilihusu maeneo ya tathmini ya athari za matukio hayo ndani ya nchi na kimataifa na ushauri wa hatua za kijamii na kisheria zinazochukuliwa ili kuimarisha amani, mshikamano wa kitaifa.

Tume inaendelea kukutana na makundi mbalimbali ikiwemo waathirika wa matukio ya uvunjifu wa amani, kwa lengo la kukusanya ushahidi na taarifa zitakazoiwezesha kuandaa ripoti ya kina.






Na Farida Mangube, Morogoro

Wafanyabiashara na walipakodi wa Wilaya ya Kilombero, mkoani Morogoro, wamepatiwa mafunzo kuhusu matumizi ya mfumo wa kielektroniki wa ukusanyaji kodi ujulikanao kama IDRAS, unaosimamiwa na Mamlaka ya mapato Tanzania (TRA).

Mafunzo hayo yametolewa na maofisa wa TRA Wilaya ya Kilombero katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, yakilenga kuwajengea uwezo walipakodi juu ya matumizi sahihi ya mfumo huo wa kidijitali.

Akizungumza katika mafunzo hayo, Meneja wa TRA Wilaya ya Kilombero Innocent Minja, amesema kuwa mfumo wa IDRAS (Mfumo Jumuishi wa Usimamizi wa Kodi za Ndani) umeanzishwa kufuatia maelekezo ya Rais wa Jamuhuri ya muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha TRA inakuwa na mifumo ya kisasa inayosomana na kuunganishwa na taasisi nyingine za serikali.

Mfumo huo ulioanza rasmi Februari 9, 2026, una uwezo wa kuruhusu mifumo mbalimbali ya kiserikali kusomana na kubadilishana taarifa kwa urahisi.

Aliongeza kuwa malengo ya kuanzishwa kwa IDRAS ni kuongeza ufanisi katika ukusanyaji wa mapato ya ndani, kuimarisha uwazi na usawa katika makadirio ya kodi, kurahisisha ulipaji wa kodi kwa njia ya mtandao, kupunguza muda na gharama ambazo walipakodi walikuwa wanatumia kufuata huduma za ana kwa ana, pamoja na kudhibiti upotevu wa mapato ya serikali kupitia mfumo jumuishi unaounganisha taasisi mbalimbali.

Kwa upande wao, washiriki wa mafunzo hayo wamesema elimu waliyoipata itawasaidia kutumia mfumo huo kwa ufanisi zaidi, kufuatilia malipo yao ya kodi kwa urahisi na kuboresha ushirikiano kati yao na TRA.

Mafunzo hayo ni sehemu ya jitihada za TRA za kuimarisha utendaji wa walipakodi na kuhakikisha mfumo wa kodi unafanya kazi kwa ufanisi zaidi katika mazingira ya kidijitali.




Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema kuwa Zanzibar inahitaji kuwa na vyuo vikuu zaidi vitakavyosaidia kuiweka Zanzibar katika ramani ya kimataifa kama kituo muhimu cha utoaji wa mafunzo na elimu ya viwango vya juu katika fani mbalimbali.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 18 Februari 2026, alipokutana na wajumbe wa Tume ya Utumishi ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wakiongozwa na Spika wa Bunge hilo, Mhe. Mussa Azan Zungu, waliofika Ikulu, Zanzibar.

Katika mazungumzo hayo, Rais Dkt. Mwinyi ameridhishwa na wazo la Bunge la ujenzi wa Chuo cha Mafunzo ya Diplomasia na Huduma za Bunge kinachotarajiwa kujengwa Zanzibar, akieleza kuwa mradi huo ni fursa adhimu kwa taifa. 

Amesema kuwa uwepo wa chuo hicho utachochea ujio wa wanafunzi na wataalamu kutoka mataifa mbalimbali kuja kujifunza Zanzibar, hali itakayochangia kukuza uchumi na kuongeza mapato ya nchi kupitia sekta ya elimu na huduma zinazohusiana nayo.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amewahakikishia wajumbe hao kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ipo tayari kushirikiana kikamilifu katika utekelezaji wa mradi huo, na kuwataka wajumbe wa Tume hiyo kulifanikisha wazo hilo kwa haraka ili Zanzibar iweze kunufaika na fursa hiyo mapema.

Kwa upande wake, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mussa Azan Zungu, amempongeza Rais Dkt. Mwinyi kwa uongozi wake thabiti ulioleta mabadiliko makubwa ya maendeleo Zanzibar, hususan katika ujenzi wa miundombinu ya barabara na kasi ya ukuaji wa uchumi inayoendana na mabadiliko ya dunia.

Wajumbe wa Tume ya Utumishi ya Bunge wako Zanzibar kwa ajili ya mafunzo ya siku tatu ya uongozi kwa Kamati ya Uongozi na Tume ya Utumishi ya Bunge, yaliyofanyika Tunguu, Mkoa wa Kusini, Unguja.









Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Iringa, Daud Yassin amesema siku 100 tangu kuingia madarakani kwa Rais, Dkt Samia zimekuwa na mwanga mkubwa wa kuleta maendeleo nchini.

Amesema kazi nyingi zimeendelea kutekelezwa huku changamoto za Watanzania zikitatuliwa kupitia sekta zote.

Akizungumza katika taarifa yake kupitia mitandao ya kijamii, Yassin amesema amani na utulivu vimeifanya Tanzania kuendelea kung'aa zaidi.

"Siku 100 za Mhe Rais Dkt Samia Suluhu Hassan zimekuwa zenye mwanga mkubwa wa maendeleo katika nchi yetu," amesema Yassin.

Yassin amesema anaungana na Watanzania wote kumtakia heri Dkt Samia na viongozi wote katika utekelezaji wa majumu yao.





Madiwani wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha mkoani Pwani wamepitisha kwa kishindo bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027 yenye jumla ya Shilingi Bilioni 68.7 katika Baraza Maalum la Madiwani lililofanyika katika Ukumbi wa Manispaa ya Kibaha.

Akizungumza wakati wa kupitisha bajeti hiyo, Mstahiki Meya wa Manispaa ya Kibaha, Dkt. Mawazo Nicas, amesema bajeti hiyo ni chachu ya maendeleo kwa wananchi na imezingatia mahitaji halisi ya Halmashauri.

“Bajeti hii imepitia kamati zote, imejadiliwa na kuboreshwa. Ni wajibu wetu kuipitisha ili ikalete maendeleo kwa wananchi wetu,” amesema Dkt. Nicas.

Diwani wa Kata ya Kibaha, Omary Bula, amesema bajeti hiyo imeandaliwa kwa ushirikishwaji wa madiwani wote na kuwataka wajumbe kuipitisha kwa maslahi ya wananchi.

Awali akiwasilisha rasimu ya bajeti hiyo, Naibu Meya wa Manispaa ya Kibaha, Aziza Mruma, amesema Halmashauri imekisia kutumia kiasi hicho cha Shilingi Bilioni 68.7, ikiwa ni ongezeko la asilimia sita ukilinganisha na bajeti ya mwaka 2025/2026.

Kwa mujibu wa Mruma, katika mchanganuo wa bajeti hiyo, mapato ya ndani yanatarajiwa kuwa Shilingi Bilioni 17.8, miradi ya maendeleo Shilingi Bilioni 8.7, huku asilimia 60 ya mapato ya ndani ikielekezwa kwenye miradi ya maendeleo na asilimia 40 kwenye matumizi ya kawaida.

Aidha, Shilingi Bilioni 1.4 zimetengwa kwa ajili ya mikopo ya vijana, wanawake na watu wenye ulemavu.

Katika mwaka huo wa fedha, Halmashauri inatarajia kujenga kituo kimoja cha afya na zahanati mbili, pamoja na kutekeleza miradi ya kimkakati yenye thamani ya Shilingi Bilioni 1.3. Miradi hiyo ni pamoja na ujenzi wa maegesho ya malori yenye thamani ya Shilingi Milioni 242.3, kituo cha kibiashara Mbonde, na ujenzi wa kiwanda cha kusindika nyama chenye thamani ya Shilingi Milioni 524.7.

Baada ya majadiliano, madiwani kwa pamoja waliipitisha bajeti hiyo kwa kauli moja, wakiahidi kusimamia utekelezaji wake ili kuhakikisha inaleta tija na maendeleo kwa wananchi wa Manispaa ya Kibaha.






Mkurugenzi wa Kitengo cha Mikakati na Siasa za Ulimwengu katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Thobias M. Makoba, tarehe 18 Februari 2026 amekutana na Prof. William A. L. Anangisye, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, katika ofisi za Makamu Mkuu wa Chuo zilizopo Ubungo, jijini Dar es Salaam.

Viongozi hao wawili walijadili mikakati ya kuimarisha ushirikiano kati ya Kitengo hicho kipya cha Wizara hususan katika eneo la utafiti, kujengea uwezo watumishi, kuandaa makongamano ya pamoja na mikutano ya kimataifa na namna ya kuimarisha ushirikiano na vyuo vingine vya Afrika.

Aidha Viongozi hao pia walijadili umuhimu wa kuandaa mikakati ya matumizi ya lugha ya Kiswahili kama nyenzo mojawapo ya kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia na kiuchumi.

Kwa upande wake, Prof.Anangisye alieleza utayari wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kushirikiana na Wizara ya Mambo ya nje katika kutekeleza masuala muhimu waliojadili na kukubaliana katika kikao hicho kwa manufaa ya pande zote mbili.

Naye Mkurugenzi wa Kitengo cha Mikakati na Siasa za Ulimwengu katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Thobias M. Makoba, alimshukuru Prof. Anangisye kwa mapokezi mazuri na utayari wa ushirikiano na Wizara katika kukuza Diplomasia ya uchumi.








Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Tumbaku Tanzania, Stanley Mnozya.

Na Mwandishi Wetu - Mara

Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Tumbaku Tanzania (TTB), Stanley Mnozya, ameonya kuwa bodi hiyo haitasita kuchukua hatua kali dhidi ya kampuni zilizopewa leseni ya kununua tumbaku katika wilaya ya Serengeti mkoani Mara ikiwa hazitatenda haki kwa wakulima.

“Natoa maelekezo kwa kampuni zote zinazonunua tumbaku hapa Mara zihakikishe zinatoa bei nzuri kwa wakulima,” Mnozya alisisitiza mbele ya waandishi wa habari jana Feburuari 17, 2026 alipokuwa katika ziara ya kikazi ya kutembelea masoko ya tumbaku katika mkoa huo wa Kanda ya Ziwa.


Alionya kuwa TTB itawanyang’aya leseni wanunuzi watakaojaribu kuwanyonya wakulima kwa kutoa bei ya chini kwa kisingizio cha bei ya tumbaku kushuka katika soko la dunia.


Mnozya alitaja kampuni ambazo zimepewa leseni ya kununua tumbaku katika wilaya ya Serengeti kuwa ni Alliance One na Global Leaf.


“Kamwe wasijifiche kwenye mwamvuli wa kushuka kwa bei ya tumbaku, Bodi haitasita kufuta leseni zao za ununuzi wa tumbaku. Kampuni zote zitende haki,” Bosi huyo wa Bodi ya Tumbaku Tanzania alisisitiza.


Hivyo, Mnozya alitoa wito kwa wakulima wa wilayani Serengeti kuendelea kujitokeza kuuza tumbaku waliyovuna akisema bado kuna fursa ya kunufaika kwa kupata kipato kizuri.


“Ninawahamasisha wakulima kuendelea kupeleka tumbaku waliyovuna sokoni. Wanayo fursa ya kupata kipato kwa sababu hata dola imeimarika, lakini pia kwa hali ya hewa iliyopo hapa kwa sasa, tumbaku ina ubora mzuri,” alisema Mnozya.


Alisema hivi sasa, bei ya tumbaku kwa daraja la kwanza ni dola za Kimarekani 3.02, daraja la pili ni dola 3, huku wastani wa bei ukiwa dola 1.95 (sawa na shilingi 5,169) kwa kilo moja.

Tumbaku kavu


“Kampuni za Alliance One, Global Leaf zimepewa leseni kununua Tumbaku wilayani Serengeri, lakini tuna mpango wa kuleta mnunuzi mwingine kwa wilaya ya Butiama,” Mnozya alidokeza akiwa katika ofisi za Chama Kikuu cha Ushirika cha Wakulima wa Mara (WAMACU Ltd).


Kwa upande wake, Meneja Mkuu (GM) wa WAMACU Ltd, Samwel Gisiboye, alimpongeza Mkurugenzi MKuu huyo wa TTB kwa kufanya ziara ya kikazi katika mkoa huo na kuahidi kuwa ushirika huo utaendelea kushirikiana na Bodi hiyo kwa ustawi wa maendeleo ya kilimo cha tumbaku na kuinua uchumi wa wakulima wa zao hilo la biashara.


GM Gisiboye alisema maandalizi yote muhimu kwa ajili ya ununuzi wa tumbaku kwa mwaka huu wa 2026 yamekamilika katika mkoa wa Mara.


“Kwanza ufunguzi wa masoko ulishafanyika katika wilaya ya Serengeti na tunaendelea kuhimiza wakulima kuendelea kuleta mitumba (robota za tumbaku) kwenye masoko,” alisema.


Hadi sasa, wilaya ya Serengeti inaongoza kwa uzalishaji wa zao la tumbaku katika mkoa huo.


Tumbaku ni moja ya mazao yanayoongoza kuingiza fedha za kigeni kwa maendeleo ya taifa, kwa mujibu wa taarifa zilizopo.


Kwa mwaka huu, bei ya tumbaku imeshuka katika soko la dunia baada ya uzalishaji wa zao hilo kuongezeka zaidi duniani na hivyo kuwa na ziada zaidi ya mahitaji.


Taarifa zinasema uzalishaji wa tumbaku kwa mwaka jana (2025) ulifikia takribani tani bilioni 5.8 dhidi ya tani bilioni 5.2 ambazo ni mahitaji ya zao hilo kwa dunia nzima.
-Aagiza Ufuatiliaji Mkali Wanaojipa Miradi TARURA


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema haikubaliki kwa watendaji wa Serikali kupokea fedha za utekelezaji wa miradi kisha kushindwa kuzitumia kwa wakati, hali inayosababisha wananchi kukosa huduma na maendeleo yaliyokusudiwa.

Dkt. Mwigulu ametoa kauli hiyo leo Februari 18, 2026, alipokuwa akizungumza na wananchi wa Ndungu, Wilaya ya Same, mkoani Kilimanjaro, ambapo ameanza ziara ya kikazi mkoani humo.

Amesema Rais Samia Suluhu Hassan amekuwa akifanya juhudi kubwa kutafuta fedha kwa ajili ya miradi ya maendeleo, hivyo ni wajibu wa watendaji kuhakikisha fedha hizo zinatumika kwa uadilifu na kwa wakati ili wananchi wanufaike.

Aidha, Waziri Mkuu amemtaka Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Reuben Kwagilwa, kufanya ufuatiliaji wa kina kubaini iwapo kuna baadhi ya watendaji wa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) wanaotumia makampuni yao binafsi kutekeleza miradi na kushindwa kusimamia ipasavyo utekelezaji wake.

Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu amesema Rais Samia ameelekeza kuwa kila kwenye eneo halali la Mtanzania lisichukukiwe bure kwa kuwa huo ndio urithi wake.

Waziri Mkuu pia amekagua maendeleo ya ujenzi wa barabara ya Ndungu–Mkomazi yenye urefu wa kilomita 36 inayojengwa kwa kiwango cha lami, mradi unaolenga kuboresha miundombinu ya usafirishaji na kuchochea shughuli za kiuchumi katika ukanda huo.

Katika hatua nyingine Waziri Mkuu ameziagiza Serikali katika vijiji kuhakikisha wanazingatia matumizi bora ya ardhi. “Kila mmoja aheshimu matumizi bora ya ardhi, na wote wanaofanya kiburi tutashughulika nao maana wanatupeleka katika kuondoa upendo miongoni mwetu”.









Top News