Benki ya Equity Bank Tanzania imeungana na wadau mbalimbali katika maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Biashara Ndogo, Ndogo na za Kati (SME Day) yaliyofanyika katika Ukumbi wa NSSF Mafao House, Ilala, Dar es Salaam, ambapo ilishiriki kama mshirika na mfadhili wa hafla hiyo iliyoandaliwa na SIDO.

Katika hafla hiyo, Equity Bank Tanzania na SIDO zilisaini Hati ya Makubaliano (MoU) ya kimkakati yenye lengo la kuwawezesha zaidi ya wajasiriamali 8,000 nchini Tanzania kupitia huduma za kifedha, mafunzo ya biashara, ushauri wa kitaalamu na uunganishaji wa masoko, ili kuimarisha ukuaji wa wa biashara ndogo na kati zinazochangia uchumi na ajira nchini 

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Bi. Theresia Aloyce Mayanie, Mkuu wa Kitengo cha Wateja Wadogo, wa Kati,  na Binafsi kutoka Equity Bank Tanzania, alisema benki hiyo itaendelea kuwa mshirika mkuu wa maendeleo ya wajasiriamali nchini kupitia suluhisho mbalimbali za kifedha. Bi. Theresia alisema: "Equity Bank tunaamini kuwa wajasiriamali ndio injini ya ukuaji wa uchumi. 

Kupitia ushirikiano wetu na SIDO, tunalenga kuwawezesha maelfu ya wafanyabiashara kupata mitaji, maarifa na fursa zitakazowasaidia kukuza biashara zao na kuboresha maisha yao.

Kwa ujumla, benki hiyo imeahidi kuendelea kushirikiana na taasisi za serikali na sekta binafsi ili kuimarisha mazingira ya biashara na kusaidia ukuaji endelevu wa wajasiriamali nchini Tanzania. @equitybanktz








●Samwel Emmanuel asema gari hilo litamsaidia kumalizia masomo, kuanzisha kipato na kusaidia familia
 
Na Mwandishi Wetu. 

Mwanza, Tanzania, 26 Juni 2026 – PigaBet imemkabidhi Samwel Emmanuel, mwanafunzi wa mwaka wa tatu katika Chuo Kikuu cha SAUT Mwanza, gari aina ya Toyota IST aliloshinda kupitia kampeni ya Shinda Ndinga.

Makabidhiano hayo yamefanyika jijini Mwanza, ambako Samwel anaishi na kusoma. Kabla ya kukabidhiwa gari hilo, Samwel alisafiri kwa ndege kwa mara ya kwanza kwenda Dar es Salaam kukamilisha taratibu za nyaraka za umiliki.

Samwel, mwenye umri wa miaka 24, ni mwanafunzi wa mwaka wa tatu anayesomea Procurement, Logistics and Supply Chain Management katika SAUT Mwanza. Ametokea Wilaya ya Busega mkoani Simiyu.

Kwa mujibu wa Samwel, taarifa za ushindi wake zilipokelewa kwa mshangao mkubwa na familia yake pamoja na marafiki zake, kwa kuwa hawakuamini mara moja kuwa ameshinda gari kupitia kampeni hiyo.

“Nilipopigiwa simu, nyumbani hawakuamini,” alisema Samwel. “Baada ya kuthibitisha taarifa, furaha ilikuwa kubwa sana.”

Samwel alisema mama yake na bibi yake walikuwa wakimpigia simu mara kwa mara kufuatilia safari yake na kuhakikisha kila hatua inaenda vizuri.

“Bibi na mama hawakulala. Walikuwa wananipigia simu kila mara kujua kama kweli naenda kuchukua gari,” alisema.

Akizungumzia ushindi huo, Samwel alisema gari hilo ni mwanzo wa hatua mpya katika maisha yake, hasa baada ya kumalizia miezi miwili iliyobaki katika masomo yake.

“Najisikia furaha kubwa sana. Siwezi kuelezea furaha niliyonayo. Namshukuru Mungu,” alisema Samwel. “Nitamalizia masomo yangu, kisha gari nitalitumia kwa biashara. Nataka linisaidie mimi na familia yangu.”

Samwel alisema mpango wake ni kulitumia gari hilo kwenye biashara ya taxi kwa kuajiri dereva ili liweze kumuingizia kipato. Pia ana ndoto ya kuwekeza kwenye kilimo na biashara ya mazao, ikiwemo mahindi na mpunga.

Arthur Kazola, Meneja Masoko wa PigaBet, alisema kampeni ya Shinda Ndinga ni sehemu ya juhudi za kampuni kuwashirikisha na kuwazawadia wateja wake.

“Tunampongeza Samwel Emmanuel kwa ushindi huu. Simulizi yake imeonesha namna kampeni hii ilivyogusa maisha ya mshindi na familia yake. Kwetu, hii siyo tu makabidhiano ya gari; ni furaha ya mshindi, familia yake na jamii inayomzunguka,” alisema Kazola.

PigaBet ilimpongeza Samwel na kuwashukuru wateja wote walioshiriki kampeni ya Shinda Ndinga.
Mwakilishi wa PigaBet, Gideon Magana (kushoto), akimkabidhi gari aina ya Toyota IST mshindi wa kampeni ya Shinda Ndinga, Samwel Emmanuel (kulia), ambaye ni mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine Tanzania (SAUT), jijini Mwanza. Samwel amesema gari hilo litamsaidia kumalizia masomo yake, kuanzisha shughuli za kujiongezea kipato, pamoja na kuisaidia familia yake.
Samwel Emmanuel akifurahia gari lake aina ya Toyota IST baada ya kukabidhiwa rasmi na PigaBet jijini Mwanza kupitia kampeni ya Shinda Ndinga.
Gideon Magana, mwakilishi wa PigaBet (kushoto) akimkabidhi Samwel Emmanuel, mwanafunzi wa SAUT Mwanza, nyaraka za gari aina ya Toyota IST aliloshinda kupitia kampeni ya Shinda Ndinga ya PigaBet, jijini Mwanza.

▪️Ni Mkutano mkubwa wa Madini na Uwekezaji

▪️Washiriki 2000 kutoka mataifa 50 Duniani kushiriki

▪️Kauli Mbiu ya Mkutano inalenga kuongeza thamani madini kwa maendelezo ya Viwanda

▪️Serikali na Sekta Binafsi kushirikiana kuandaa mkutano huo

▪️Waziri Mavunde azindua rasmi maandalizi ya mkutano huo

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Dkt. Samia S. Hassan anatarajiwa kufungua rasmi Mkutano wa Saba wa Madini na Uwekezaji Tanzania (TMIC 2026) utakaofanyika Novemba 19 hadi 21, 2026 katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam.

Akizungumza leo Juni 27, 2026 wakati wa uzinduzi wa TMIC 2026, Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, amesema serikali imeamua kujenga uchumi wa viwanda unaotokana na madini kwa kuwekeza katika uchakataji na uyeyushaji wa madini badala ya kuendelea kuuza malighafi.

Amesema kaulimbiu ya mkutano huo, "Madini Yaliyoongezwa Thamani: Chachu ya Ukuaji wa Viwanda na Uchumi," inaakisi dira ya serikali ya kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha uchakataji wa madini barani Afrika.

Kwa mujibu wa Mhe. Mavunde, amesema Tanzania tayari ina viwanda vinane vya kusafisha dhahabu, huku Mkoa wa Dodoma ukiwa na viwanda tisa vinavyojengwa na vinavyoendelea na uzalishaji pamoja na kiwanda kikubwa cha kuyeyusha madini ya nikeli na shaba.

"Zaidi ya Sh bilioni 600 zinawekezwa katika ujenzi wa kiwanda cha chuma kitakachotumia asilimia 100 ya malighafi za ndani, huku uwekezaji mwingine ukiendelea Kigamboni na Tanga kwa ajili ya uchakataji wa madini ya 'Heavy Mineral Sands' na mradi wa madini ya niobium wa Panda Hill, Mbeya," amesema Mhe. Mavunde

Amesema, katika kuongeza ushiriki wa Watanzania kwenye sekta hiyo,  thamani ya manunuzi kupitia mpango wa 'Local Content' imefikia Sh trilioni 5.1, huku bidhaa 20 zikitakiwa kuzalishwa na wazawa kwa ajili ya kuhudumia migodi mikubwa.

 Amesisitiza wafanyabiashara kuzingatia uaminifu na viwango vya kimataifa ili kunufaika zaidi na fursa hizo.

Amesema sekta ya madini imeendelea kuimarisha mchango wake katika uchumi kwa kuingiza Sh trilioni 1.374 katika Mfuko Mkuu wa Serikali, kiwango kilichovuka lengo la Sh trilioni 1.2 kwa mwaka huu wa fedha.

Mhe. Mavunde, amesema Serikali imeidhinisha asilimia 10 ya mapato yote ya sekta ya madini kuelekezwa kwenye utafiti wa kina wa jiofizikia ili kuongeza maeneo yanayofahamika kuwa na madini kutoka asilimia 16 ya sasa hadi asilimia 50 ifikapo mwaka 2030.

Aidha, amesema Serikali inaandaa mfuko maalumu wa mikopo kwa wachimbaji wadogo, ambao licha ya changamoto za mitaji na teknolojia, wanachangia takribani asilimia 40 ya mapato ya sekta ya madini.

Katika hatua nyingine, amesema Serikali inaanza operesheni ya kufuta kidijitali leseni zote za madini zisizotumika. Wamiliki watakaoshindwa kuwasilisha taarifa ndani ya muda uliowekwa watapewa notisi ya siku 30 kabla ya leseni hizo kujifuta moja kwa moja.

Nae, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Mhandisi Yahya Samamba, amesema Serikali imejipanga kuhakikisha utajiri wa madini unakuwa chachu ya kukuza viwanda vya ndani, kuongeza ajira na kuimarisha uchumi kupitia uongezaji thamani badala ya kuishia kwenye uchimbaji pekee.

Amesema TMIC 2026 utawakutanisha viongozi wa Serikali, taasisi za fedha, kampuni za madini, wataalamu wa teknolojia, watafiti na wadau wengine kutoka duniani kote kujadili fursa za uwekezaji na maendeleo ya sekta hiyo.

 "Huu ni wakati wa kuingia katika awamu mpya ya uwekezaji, ubunifu na ukuaji wa sekta ya madini nchini," amesema.

Kwa upande wa Katibu Mtendaji wa Chemba ya Migodi Tanzania, Mhandisi Benjamin Mchwampaka, amesema mkutano huo unatarajiwa kuwakutanisha washiriki zaidi ya 2,000 na watoa mada zaidi ya 100 kutoka mataifa zaidi ya 50, huku zaidi ya mada 20 zikijadiliwa zikiwemo sera, kodi, uwekezaji, teknolojia, nishati safi, madini ya kimkakati, uongezaji thamani na masuala ya mazingira, jamii na utawala bora (ESG).

Mchwampaka amesema TMIC 2026 pia utaweka mkazo katika maendeleo ya wachimbaji wadogo pamoja na ushirikishwaji wa wanawake na watu wenye ulemavu katika mnyororo mzima wa uongezaji thamani wa madini. Mkutano huo unatarajiwa kufungwa rasmi na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi.












Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Dodoma Juni 27, 2026, imefanya matembezi ya hisani kutoka ofisi za TRA hadi uwanja wa Kilimani pamoja na bonanza la michezo ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 30 ya TRA na maandalizi ya kuelekea Tuzo za Mheshimiwa Rais kwa Walipakodi, Julai 1, 2026.

Akizungumza katika hafla hiyo, Meneja wa TRA Mkoa wa Dodoma, Pendolake Elinisafi, amesema TRA imepata mafanikio makubwa tangu kuanzishwa kwake mwaka 1996, ikiwemo kuboresha huduma kwa walipakodi, kuongeza matumizi ya teknolojia katika ukusanyaji wa mapato na kuimarisha uhusiano na walipakodi.

Amesema maadhimisho ya miaka 30 yanaongozwa na kaulimbiu isemayo, “Miaka 30 ya TRA, Kulipa Kodi ni Uzalendo na Ushujaa kwa Maendeleo na Kujitegemea kwa Taifa Letu”, ameongeza kuwa TRA Dodoma kuelekea kilele cha miaka 30 kwa kutekeleza shughuli za uwajibikaji kwa jamii, zikiwemo upandaji miti katika Shule ya Sekondari Miyuji, matembezi ya hisani na bonanza la michezo.

Kwa upande wake Mgeni rasmi ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Mpwapwa Dkt. Sophia Kizigo, ameipongeza TRA kwa kuendelea kuboresha huduma kwa walipakodi na kusimamia ukusanyaji wa mapato kwa uadilifu, pia amempongeza Meneja wa TRA Mkoa wa Dodoma, Pendolake Elinisafi, kwa uongozi wake katika kuimarisha mazingira rafiki kwa walipakodi na usimamizi wa ukusanyaji wa mapato mkoani humo.

Dkt. Kizigo ameeleza ushirikiano unaojengwa kupitia shughuli za kijamii unaongeza uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa kulipa kodi na kuimarisha imani kwa TRA, amewahimiza watumishi wa TRA kuendelea kufanya kazi kwa weledi na uadilifu, pamoja na walipakodi kuendelea kutimiza wajibu wao kwa maendeleo ya Taifa.

Maadhimisho hayo pia yamehusisha zoezi la uchangiaji damu kwa ajili ya kusaidia wanawake wajawazito, watoto na wanaohitaji huduma za dharura pamoja bonanza la michezo lililojumuisha mpira wa miguu, kuvuta kamba,kukimbia ndani ya gunia, kukimbia na yai na kukimbiza kuku, huku matembezi ya hisani yakiwakutanisha watumishi wa TRA na baadhi ya walipakodi kuimarisha mshikamano na ushirikiano.










Na Mwandishi Wetu
HOSPITALI ya Shifaa imeanzisha madarasa kwaajili ya kutoa elimu kuhusu umuhimu wa lishe bora na mtindo wa maisha ikiwa ni jitihada za kukabiliana na changamoto ya kisukari ambacho kimekuwa chanzo cha magonjwa mengi sugu.

Hayo yamesemwa leo, Juni 26, 2026 jjijini Dar es Salaam na Daktari bingwa mbobezi wa homoni na tezi wa Hospitali ya Shifaa ya Kinondoni, Dkt. Singla Mosha, wakati akizungumzia magonjwa sugu

Amesema miongoni mwa maradhi wanayotibu ni kisukari na kwamba kitu cha muhimu ambacho wamekuwa wakitilia mkazo ni kutambua kuwa shida ya ugonjwa wa kisukari ndiyo msingi wa matatizo mengi ya kiafya.

Amesema Katika matibabu ya sukari na magonjwa mengine sugu, eneo ambalo halijapewa nafasi yake ipasavyo na msisitizo wa kutosha ni suala la lishe na mtindo wa maisha.

Amesema Shifaa imejikita sana katika kuonesha umuhimu wa lishe na mtindo wa maisha katika kukabiliana na changamoto hiyo ya kisukari ambacho ndicho chanzo cha matatizo mengi ya maradhi sugu kwenye jamii.

Ametoa mfano kuwa sukari ndiyo imekuwa changamoto ya mafuta kwenye ini, maradhi ya kushindwa kupata ujauzito, uzito uliopitiliza, kiharusi, maradhi ya moyo, maradhi ya figo na mengineyo.

“Maradhi hayo yote niliyotaja ukiangalia kwa sehemu kubwa kabisa chanzo chake ni maradhi ya kisukari ambayo chanzo chake hasa ni shida ya lishe isiyo sahihi na mtindo mbovu wa maisha,” amesema na kuongeza

“Ukiaangalia muda ambao mgonjwa anakutana na daktari hautoshi kufahamishwa kuhusu mtiririko wa mtindo wake wa maisha na lishe kwa hiyo Shifaa imeanzisha madarasa ambayo tunafanya kama sehemu kamili ya kuonana na daktari ambapo watakaa kwa muda mrefu kuzungumza,” alisema

Amesema Shifaa imeanzisha madarasa hayo kwaajili ya kuwaelimisha wagonjwa ambao inawahudumia kwenye maeneo ambayo hayajapewa msisitizo wa kutosha ambayo ni lishe na mtindo wa maisha.

Amesema kwa kipindi ambacho wameshafanya madarasa hayo wameshaona matokeo makubwa sana kwenye matokeo ya wagonjwa waliokuwa wakiwahudumia

Dkt. Mosha Amesema elimu ya afya kwenye mitandao ya kijamii imekuwa ikiwachanganya watu kwani wengi wanaofanya hivyo hawana utaalamu wa kutosha wa masuala ya afya, wala namna ya kuthibitsha ufanisi na usalama wa ushauri wao, kwani wanafanya hivyo kama biashara.

“Uzuri ni kwamba hapa Shifaa ukija unaonana na daktari mtaalamu wa eneo hilo, tuna maabara yenye ubora wa hali ya juu kabisa, ambayo utapimwa kuthibitisha kuwa mafunzo tunayokupa yanakusaidia au la… Siyo kupewa ushauri tu ukishakutana na daktari unapimwa kuona mabadiliko ya afya yako,” amesema.

“Tumekuwa tukiwahudumia wagonjwa wa kisukari aina ya pili, sisi tunasuluhisho la kumpungizia mgonjwa mzigo wa dawa anazolazimika kutumia kwa siku, tumekuwa na wagonjwa waliopimwa na kuonekana wana kisukari aina ya pili lakini tumewaondoa kwenye matumizi ya dawa,” amesema



DODOMA: Serikali imesema haijauza wala haijakabidhi rasilimali za misitu au maliasili za Tanzania kwa mataifa ya nje kupitia makubaliano ya biashara ya kaboni, ikisisitiza kuwa hatua zinazoendelea zinalenga kuongeza manufaa ya kiuchumi kwa taifa huku zikilinda maslahi ya wananchi.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Juni 26, 2026 jijini Dodoma, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhandisi Hamad Yussuf Masauni, amekanusha madai yaliyotolewa na baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani, akieleza kuwa taarifa zinazodai serikali imekabidhi maliasili kwa wawekezaji wa nje si za kweli na zinapotosha umma.

Alisema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeweka msingi wa kisheria na kiutawala wa kusimamia biashara ya kaboni ili kuhakikisha Tanzania inanufaika na soko la kimataifa la biashara hiyo.

Kwa mujibu wa Mhe. Masauni, bajeti ya mwaka wa fedha wa sasa imetenga fedha kwa ajili ya kuanzisha mifumo ya usajili, ukaguzi na ufuatiliaji wa biashara ya kaboni. Alieleza kuwa mifumo hiyo itasaidia kudhibiti shughuli zote zinazohusiana na biashara hiyo na kuhakikisha mapato yanayostahili yanapatikana kwa mujibu wa sheria.

Aidha, alisema serikali imeunda kamati ya wataalamu kutoka wizara mbalimbali ili kupitia fursa zilizopo katika sekta ya biashara ya kaboni na kupendekeza namna bora ya kuongeza manufaa kwa taifa bila kuhatarisha uhifadhi wa mazingira na rasilimali za asili.

Akizungumzia ushirikiano wa Tanzania na mataifa mbalimbali, Mhe. Masauni alisema makubaliano yaliyofikiwa na nchi kama Oman, Singapore, Japan na Korea yanahusu ushirikiano wa kiuchumi na kufungua masoko ya biashara, badala ya kuhamisha umiliki wa rasilimali za Tanzania.

Alisisitiza kuwa hakuna makubaliano yanayoruhusu taifa jingine kumiliki au kusimamia maliasili za Tanzania, akibainisha kuwa rasilimali zote za nchi zitaendelea kulindwa kwa mujibu wa Katiba na sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mhe. Masauni aliwataka wananchi kupuuza taarifa za upotoshaji kuhusu biashara ya kaboni na kufuatilia taarifa rasmi za serikali, akieleza kuwa hatua zinazochukuliwa zinalenga kuhakikisha Tanzania inanufaika zaidi na fursa za soko la kimataifa huku ikihifadhi mazingira na kuongeza mapato ya taifa.

 

Serikali ya Tanzania imeingia makubaliano na kampuni mbili kutoka Japan kwa ajili ya kufungua fursa za soko la biashara ya kaboni kupitia mpango wa Uratibu wa Pamoja wa Mikopo (JCM), hatua inayolenga kuongeza mchango wa sekta binafsi katika kufanikisha dira ya taifa ya maendeleo ya mwaka 2050.

Akizungumza katika warsha ya kusaini Hati ya makubaliano hayo, Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Dkt. Richard Mayungi, alisema serikali ina jukumu la kuhakikisha dira ya 2050 inafikiwa kupitia uwekezaji katika nishati safi, biashara ya kaboni na udhibiti wa taka.

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa Kituo cha Biashara ya Kaboni (NCMC), Ngenda Kigaraba, alibainisha kuwa utoaji wa mikopo kwa pamoja utasaidia kulinda mazingira, kukuza biashara na kuongeza mapato ya Serikali.

Naye Afisa Mtendaji Mkuu wa kampuni ya 3T kutoka Japan, Kan Shimizu, alisema Tanzania itanufaika kwa kiasi kikubwa kupitia ushirikiano huu, hususani katika sekta ya utunzaji wa mazingira na biashara ya kaboni

Makubaliano haya ya ushirikiano kati ya NCMC na kampuni za Japan yanalenga kuchochea mchango wa sekta binafsi katika kufanikisha malengo ya Dira ya taifa ya mwaka 2050, ambapo nguzo ya tatu ya Dira hiyo inasisitiza ukuaji wa uchumi wa Taifa na maendeleo endelevu yanayozingatia mazingira endelevu.


Top News