Katika kuelekea kilele cha maadhimisho ya Jubilei ya Dhahabu ya miaka 50 ya Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), mwaka huu wadau wa biashara, wawekezaji, wabunifu na wananchi wanatarajiwa kushuhudia tukio la kipekee la kihistoria litakalojulikana kama “Sabasaba Golden Night”, Usiku wa Tuzo utakaofanyika tarehe 6 Julai 2026, usiku huu maalum wa dhahabu unalenga kusherehekea mafanikio, ubunifu na mchango wa maonesho hayo katika kukuza biashara na uchumi wa Tanzania kwa zaidi ya nusu karne.

Aidha,Uzinduzi wa Sabasaba Golden Night umebeba taswira mpya ya Maonesho ya Sabasaba ya mwaka 2026, ukiahidi burudani ya kiwango cha juu, mwangaza wa kipekee, maonesho ya kisasa, kutambua wadau waliotoa mchango mkubwa katika safari ya miaka 50 pamoja na kuunganisha sekta za biashara, uwekezaji na ubunifu chini ya jukwaa moja. Tukio hilo linatarajiwa kuwa moja ya vivutio vikubwa ndani ya Maonesho ya 50 ya Jubilei ya Dhahabu, yakiyotarajiwa kufanyika kuanzia tarehe 28 Juni hadi 13 Julai, 2026.

Akizungumza Mgeni Rasmi Mhe. Dennis Londo amesema Tuzo hizo zitakazotolewa Mwaka huu zinalenga kuonesha ni kwa namna gani Sekta ya Biashara imekua kupitia maonesho ya Biashara ya Sabasaba na namna ambavyo Maonesho haya yamekuza maelfu ya wafanyabiashara amba sasa ni wakubwa.

Aidha Dkt.Latifa Mohammed Khamis Mkurugenzi Mkuu wa Maendeleo ya Biashara Tanzania ameeleza kuwa “Usiku wa Dhahabu” si burudani pekee, bali ni ishara ya heshima kwa safari ya mafanikio ya Sabasaba tangu kuanzishwa kwake, sambamba na kufungua ukurasa mpya wa fursa za biashara, teknolojia na ushirikiano wa kimataifa. Wageni watakaohudhuria watapata nafasi ya kushuhudia historia ikikutana na ubunifu wa kizazi cha sasa katika mazingira yatakayobeba hadhi ya Jubilei ya Dhahabu. “Sabasaba 2026 KUBWA KULIKO

Na; Mwandishi Wetu, Unguja

WAZIRI  wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni amesema msimu ujao wa Ligi ya Muungano utaboreshwa zaidi ikiwa pamoja na zawadi kwa bingwa ili kuipa hadhi ya kipekee ligi hiyo.

Amesema lengo ni kuifanya ligi hiyo inakuwa moja ya ligi bora Afrika Mashariki na kuifanya kuwa na mvuto wa aina yake kwa wapenda soka akieleza kuwa michezo ndio sehemu ambayo jamii hukutana na kuongea lugha moja.

Mhe. Masauni ameyasema hayo Mei, 24, 2026 Unguja, Zanzibar wakati wa halfa ya utoaji tuzo na zawadi kwa walioshiriki na kufanikisha Ligi ya Muungano 2026 ambapo Simba ilitawazwa mabingwa kwa kuifunga Yanga bao 1-0 katika mchezo uliochezwa Uwanja wa Amaan Complex.

“Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar zimeendelea kuchukua hatua madhubuti za kuimarisha Muungano kwa misingi ya Kikatiba, Kihistoria, Mshikamano wa Kitaifa na maendeleo ya pamoja.

“Juhudi hizo zinajielekeza kuhakikisha kuwa jamii ya Watanzania inakuwa na umoja na ushirikiano katika nyanja zote za kiuchumi, kijamii na kisiasa.

Mhe. Masauni amesema, Ofisi ya Makamu wa Rais ambayo ndiyo yenye dhamana na masuala ya Muungano kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeamua kuwa sehemu ya uratibu wa Ligi ya Muungano ili kuongeza nguvu.

Amesema hatua hii itasaidia kuboresha maandalizi ya ligi ikiwemo kuboresha zawadi kwa washiriki na mshindi wa ligi.

“Nizipongeze timu zote ambazo zilishiriki mashindano haya kwa mwaka 2026 maana ushiriki wao ndio mafanikio ya uwepo wa Ligi hii ya Muungano.”

Kwa upande wake, Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo Zanzibar, Dkt. Riziki Pembe Juma amesema pamoja na ligi hiyo kusimama kwa muda mrefu lakini ilipotangazwa kurejea wadau waliitikia vizuri na kutoa ushirikiano.

“Awali kama wizara tulianza kwa wasiwasi lakini mwisho tulimaliza kwa furaha kwani tumegundua michezo imekuwa kitu cha kipekee na tutazidi kushirikiana na kumalizika kwa msimu huu inafanya tuanze maandalizi kwa ajili ya mwaka ujao,” amesema Mhe. Dkt. Riziki.

Naye, Katibu Mkuu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Zanzibar (ZFF), Hussein Ahmada amezishukuru serikali za pande zote mbili kwa kuifanya michezo kuwa moja ya eneo la kuwaunganisha Watanzania kupitia Ligi ya Muungano akieleza kuwa hali hiyo imekuwa faraja kwa wapenda soka kuona nao wanathaminiwa.

Mwaka huu ligi hiyo ilishirikisha timu nane ambazo ni Simba iliyotwaa ubingwa, Yanga, Azam na Singida Black Stars kutoka Tanzania Bara wakati kwa Zanzibar ilikuwa Mlandege, KVZ, Mafunzo na Muembe Makumbi.


Na Janeth Raphael MichuziTv Bungeni- Dodoma.

Serikali imesema kuwa Makao yote ya Watoto nchini yanaanzishwa na kuendeshwa kwa kuzingatia sheria, kanuni na miongozo maalum inayolenga kuhakikisha watoto wanaolelewa katika vituo hivyo wanaishi katika mazingira salama, yenye ulinzi na malezi bora.

Kauli hiyo imetolewa leo Mei 25, 2026 bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Maryprisca Winfried Mahundi wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Lucy Simirya Kombani ambaye alitaka kujua ni utaratibu gani unaotumiwa na Serikali kuhakikisha watoto wanaoishi katika vituo vya kulelea watoto wanapata mazingira bora na salama.

Akijibu swali hilo, Mahundi amesema Makao yote ya Watoto yanaanzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Mtoto Sura ya 13, Kanuni za Makao ya Watoto za mwaka 2012 pamoja na Mwongozo wa Taifa wa Uanzishaji, Uendeshaji na Usimamizi wa Makao ya Watoto wa mwaka 2024.

Amesema utaratibu wa kuanzisha Makao ya Watoto huanzia ngazi ya Kata ambapo maombi hupokelewa na kufanyiwa tathmini kabla ya kuwasilishwa katika ngazi ya Halmashauri na hatimaye kupelekwa Wizarani kwa Kamishna wa Ustawi wa Jamii kwa ajili ya kupata leseni ya usajili.

“Makao hayo hupatiwa usajili rasmi pale yanapokidhi vigezo na masharti yote yaliyowekwa na Serikali kwa ajili ya kuhakikisha watoto wanapata huduma stahiki za malezi, ulinzi na maendeleo yao kwa ujumla,” amesema Mahundi.

Aidha, Naibu Waziri huyo ameeleza kuwa Serikali imeendelea kuimarisha usimamizi wa Makao ya Watoto kupitia Maafisa Ustawi wa Jamii waliopo katika ngazi mbalimbali kuanzia Wizara, Mkoa hadi Halmashauri.

Kwa mujibu wa Mahundi, Maafisa hao hufanya ukaguzi na ufuatiliaji wa mara kwa mara katika vituo vya kulelea watoto ili kuhakikisha huduma zinazotolewa zinazingatia viwango vya ubora pamoja na kulinda haki na usalama wa watoto wanaolelewa humo.

Amesisitiza kuwa Serikali haitaruhusu uwepo wa Makao ya Watoto yanayokiuka taratibu, sheria na miongozo iliyowekwa kwani lengo kuu ni kuhakikisha watoto wote wanaopata huduma katika vituo hivyo wanalelewa katika mazingira yenye upendo, usalama na ustawi unaostahili.

Kauli hiyo imekuja wakati Serikali ikiendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha mifumo ya malezi na ulinzi wa watoto nchini, sambamba na kuhakikisha taasisi zote zinazohusika na huduma za watoto zinafanya kazi kwa kuzingatia sheria na misingi ya haki za mtoto.




Na Ashura Mohamed, Karatu


Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) imeridhishwa na hatua iliyofikiwa katika utekelezaji wa Mradi wa Utafiti wa Mafuta na Gesi wa Eyasi-Wembere uliopo Wilaya ya Karatu, Mkoa wa Arusha.

Ziara hiyo ya ukaguzi iliongozwa na Mwenyekiti wa Bodi ya TPDC, Balozi Ombeni Sefue, ambaye alisema shirika limepiga hatua kubwa kwa kuhakikisha kazi nyingi za kitaalamu sasa zinafanywa na wataalamu na wakandarasi wazawa wa Kitanzania.

Kwa mujibu wa Balozi Sefue, awali baadhi ya kazi hizo zilikuwa zikifanywa na makampuni ya nje ya nchi, lakini sasa TPDC imeweka mkazo kwa wazawa ili kujenga uwezo wa kitaalamu ndani ya nchi.

“Kazi nyingi za kitaalamu sasa zinafanywa na vijana waliopo hapa nchini kwa ubora unaotakiwa ikiwa ni pamoja na wakandarasi wazawa ambao wameajiriwa na TPDC,” alisema Balozi Sefue.

Akizungumzia matumizi ya fedha katika mradi huo, Balozi Sefue alibainisha kuwa hadi sasa zaidi ya shilingi bilioni 47 zimetumika tangu mradi uanze mwaka 2015 hadi mwaka 2026. Alifafanua kuwa fedha hizo zimetoka ndani ya TPDC, kutokana na imani kuwa utafiti huo utatoa matokeo chanya yatakayonufaisha taifa.

“Sasa utafutaji wa mafuta una hatua nyingi kwa sababu ni gharama kubwa sana kuchimba visima vya mafuta. Huwezi kuanza kuchimba kabla ya kufanya hatua ya kwanza ikakupa matumaini, halafu unaenda hatua ya pili na ya tatu mpaka mwisho unachimba kisima cha majaribio ili kupata matokeo chanya,” alieleza.

Balozi Sefue alitaja changamoto zinazokabili mradi huo kuwa ni pamoja na eneo la Ziwa Eyasi kuwa na tope na wakati mwingine ziwa kuka, hali inayochelewesha utekelezaji wa kazi licha ya mkandarasi kuwa na vifaa vya kisasa.

Kwa upande wake, Meneja wa Mradi wa Eyasi-Wembere, kutoka TPDC,Sindi Maduhu, alisema sasa mradi upo katika hatua ya kuchukua data za mitetemo na wanatarajia kukamilisha awamu ya kwanza ifikapo mwezi Juni 2026.

Aliongeza kuwa kazi hiyo inatekelezwa na mkandarasi mzawa, Kampuni ya African Geophysical Service (AGS), ambayo imepata mafanikio makubwa kutokana na matumizi ya wataalamu wenye ujuzi na mitambo ya kisasa inayolingana na mazingira ya eneo hilo.

Mradi wa Eyasi-Wembere unapitiwa pia na bomba la mafuta la Afrika Mashariki (EACOP), jambo linalotarajiwa kuwezesha usafirishaji wa mafuta yatakayopatikana na kuongeza kasi ya shughuli za utafiti katika eneo hilo.
Meneja wa mradi kutoka TPDC Sindi Maduhu akitoa maelekezo kwa Kamati ya Bodi ya Wakurugenzi TPDC


Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi TPDC Balozi Ombeni Sefue akiwa katika Ziwa Eyasi wakati wa Ukaguzi wa MRADI WA Eyasi-Wembere



Na Mwandishi Wetu
SHULE ya St Anne Marie Academy iliyoko Mbezi Kimara kwa Msuguri jijini Dar es Salaam mwaka huu inatimiza miaka 25 yenye mafanikio makubwa kwenye utoaji wa elimu bora tangu kuanzishwa kwake.

Tarehe 18 Julai mwaka huu itatimiza miaka 25 ikiwa ni miongoni mwa shule bora nchini ambazo zimekuwa zikifanya vizuri kwenye matokeo ya kitaaluma kuanzia ngazi ya kata, Wilaya, Mkoa hadi kwenye ngazi ya taifa.

Hayo yalisemwa mwishoni mwa wiki na Mbunge wa Bukoba Vijijini (CCM), ambaye pia ni Mkurugenzi Mwanzilishi wa shule hizo Dkt. Jasson Rweikiza wakati akizungumza kuhusu miaka 25 ya kutoa huduma ya elimu.

Dkt Rweikiza alisema miongoni mwa mafanikio makubwa ya shule hiyo kwa miaka 25 ni kutoa mwanafunzi bora kitaifa katika matokeo ya darasa la saba yaliyotangazwa na Baraza la Taifa la Mitihani NECTA mwaka 2021.

Alisema licha ya kutoa mwanafunzi bora kitaifa mwaka 2021, shule hiyo imekuwa ikifanikiwa kuingiza wanafunzi wengi kwenye 10 bora kitaifa kwa miaka mingi na imepata pongezi nyingi kitaifa na kimataifa.

“Upekee wa shule yetu ya St Anne Marie Academy ni kuwa na miundombinu bora kama maktaba zenye viyoyozi zilizosheheni vitabu vya kila aina, maabara za kisasa za sayansi zinazowawezesha wanafunzi wa masomo ya sayansi kusoma kwa vitendo,” alisema Dk Rweikiza.

Aidha, alisema St Anne Marie Academy ni shule ya kwanza na ya pekee nchini kuanzisha utaratibu wa kuwasomesha bure hadi kumaliza masomo yao wanafunzi wa shule hiyo wanaofiwa na mzazi anayelipa ada.

“Tumekuwa tukiahidi na kutekeleza kwamba hakuna mwanafunzi atakayefukuzwa shule kwa kukosa ada baada ya kufiwa na mzazi aliyekuwa akilipa ada, kama mwanafunzi yuko darasa la kwanza basi atasoma hadi darasa la saba na kama yuko kidato cha kwanza basi atamaliza kidato cha nne,” ni kauli ya Dk Rweikiza ambayo amekuwa akiitoa mara kwa mara kwenye mahafali shuleni hapo.

Dkt Rweikiza alisema matokeo bora ya shule hiyo ni jambo ambalo halijatokea kwa bahati bali ni kutokana na moundombinu bora iliyowekwa ikiwemo bodi ya mitihani ndani ya shule hiyo.

“Ili kuongeza ufanisi wa kitaaluma, kazi ya kutunga mitihani shuleni kwetu St Anne Marie Academy imekuwa ikifanywa na bodi hiyo ya mitihani na walimu wanakuwa na kazi ya kufundisha tu hali ambayo imeongeza ufaulu kwa kiwango kikubwa,” alisema

“Walimu wa St Anne Marie Academy tumewaachia kazi ya kufundisha tu, kazi ya kutunga mitihani ni ya bodi ya mitihani na tangu tuanzishe utaratibu huu tumeona mafanikio makubwa sana ya kuongezeka kwa ufaulu wa wanafunzi wetu,” alisema Dk Rweikiza


MBUNGE wa Viti Maalum Mkoa wa Pwani, Mariam Ibrahim, ameendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia.
Ameyasema hayo leo alipokuwa mgeni rasmi katika mashindano ya “Mkali wa Chapati” yaliyofanyika Wilaya ya Mkuranga, Mkoa wa Pwani, ambapo amesema mashindano hayo ni sehemu ya juhudi za kuhamasisha matumizi ya nishati safi chini ya uongozi wa Rais Dk.Samia Suluhu Hassan.

“Mashindano haya ni sehemu ya juhudi za kumuunga mkono Rais Dk.Samia Suluhu Hassan katika kampeni ya matumizi ya nishati safi kwa wananchi. Hakika Rais Samia ni kiongozi imara ambaye ameweka mbele maslahi ya wananchi pamoja na utunzaji wa mazingira,” amesema Mariam Ibrahim.

Aidha amewataka wananchi wa Wilaya ya Mkuranga kuachana na matumizi ya majiko ya mkaa na badala yake kutumia nishati safi kama gesi ili kupunguza ukataji wa miti na kulinda mazingira.

Pia amesema kutakuwa na mashindano mengine yajayo yakiwemo ya upishi wa pilau na nyama choma, yenye lengo la kuendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi pamoja na kukuza mshikamano wa kijamii.
Katika hatua nyingine, amewaomba wananchi wa wilaya hiyo kuendelea kushikamana na kushirikiana katika shughuli mbalimbali za kijamii kwa maendeleo ya jamii yao.

Wakati huo huo  amemshukuru Mbunge wa Jimbo la Mkuranga Abdallah Ulega, kwa kufanikisha mashindano hayo pamoja na shughuli zote zilizofanyika siku hiyo.

“Maandalizi na mafanikio ya mashindano hayo yametokana na juhudi za Mbunge Abdallah Ulega kwa kushirikiana na wananchi wa Mkuranga,”amesema.








 

Na Benny Mwaipaja, Congo, Brazaville.

Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amewasili nchini Congo, Brazzaville, amabako atashiriki Mkutano Mkuu wa 61 wa mwaka 2026 wa Bodi ya Magavana wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB) na Mkutano Mkuu wa 52 wa Mwaka wa Mfuko wa Maendeleo wa Benki hiyo (ADF), uliopangwa kufanyika kuanzia tarehe 25 hadi 29 mwaka 2026, katika Mji Mkuu wa Congo, Brazaville.
Katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Brazaville, Maya Maya, Mheshimiwa Balozi Omar, alilakiwa na Balozi wa Tanzania nchini Congo, Brazaville, Mhe. Said Juma Mshana.

Katika msafara huo, Mhe. Balozi Omar, ambaye ni Gavana wa Benki ya Maendeleo ya Afrika, ameambatana na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mlipaji Mkuu wa Serikali ambaye pia katika Muundo wa Benki ya Maendeleo ya Afrika ni Gavana Mbadala wa Benki hiyo (Alternative Governor), Dkt. Natu El-maamry Mwamba na Naibu Katibu Mkuu ambaye pia ni Kamishna wa Fedha za Nje, Bw. Rished Bade.

Zaidi ya wajumbe 3,000 kutoka nchi mbalimbali za Afrika na Kimataifa, wanatarajiwa kuhudhuria Mkutano Mkuu huo, Utakaofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Kintélé, wakiwemo Marais na Wakuu wa Serikali za Afrika, Mawaziri wa Fedha, Magavana wa Mabenki Kuu, washirika wa maendeleo, wawakilishi wa sekta binafsi, viongozi wa asasi za kiraia, wasomi, taasisi za utafiti, NGOs, na wadau wengine.

Kauli mbiu ya mwaka huu ni: “Kuhamasisha Ufadhili wa Maendeleo ya Afrika kwa Wingi katika Dunia Iliyogawanyika”. Kauli hii inasisitiza umuhimu wa kuziba pengo la kifedha linalokua kwa mahitaji ya maendeleo ya Afrika, hasa katika mazingira ya kisiasa na kiuchumi duniani yanayobadilika kwa kasi.

Mkutano pia utajadili masuala mtambuka kama mageuzi ya kidijitali, uimarishaji wa taasisi na utawala bora. Haya yote yanalingana na utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs), Mkataba wa Paris wa Mabadiliko ya Tabianchi, Ajenda 2063 ya Umoja wa Afrika, na Mikakati Mikuu Mitano ya Benki ya Maendeleo ya Afrika (High 5s).











Na Janeth Raphael MichuziTv - Iringa

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mwigulu Nchemba, ameonyesha kutoridhishwa na baadhi ya hospitali nchini kuendelea kuwaagiza wananchi kununua dawa nje ya hospitali licha ya Serikali kutoa fedha kwa ajili ya ununuzi wa dawa hizo.

Dkt. Mwigulu amesema Serikali imekuwa ikipeleka fedha nyingi katika sekta ya afya ili kuhakikisha hospitali na vituo vya kutolea huduma za afya vinakuwa na dawa za kutosha kwa ajili ya wananchi, huku taarifa za vitabu zikionyesha kuwa kiwango cha upatikanaji wa dawa kinafikia zaidi ya asilimia 90.

Hata hivyo, amesema bado wananchi wengi wanapofika hospitalini kupata matibabu huambiwa kwenda kununua dawa katika maduka binafsi jambo alilolitaja kuwa ni “mambo ya ajabu” yasiyopaswa kuendelea kuvumiliwa.

“Mtu anaambiwa dawa zipo kwa mujibu wa taarifa na kumbukumbu za hospitali, lakini mgonjwa akifika anatakiwa kwenda kununua dawa mtaani. Haya ni mambo ya ajabu kabisa na hayakubaliki,” amesema Dkt. Mwigulu.

Kutokana na hali hiyo, Waziri Mkuu amesema tayari ametoa maelekezo kwa Mganga Mkuu pamoja na watendaji wa Mkoa wa Iringa kuhakikisha dawa zote zinazonunuliwa kwa fedha za Serikali zinawafikia wananchi kama ilivyokusudiwa.

Amesisitiza kuwa viongozi na watendaji wa sekta ya afya wanapaswa kusimamia kwa karibu matumizi ya fedha zinazotolewa na Serikali ili kuondoa changamoto zinazowakabili wananchi wanapohitaji huduma za matibabu.

“Natoa maelekezo kwa Mganga Mkuu pamoja na watendaji wote kuhakikisha dawa zitakazotumika katika hospitali zote za Mkoa wa Iringa zinasimamiwa ipasavyo. Mimi mambo ya ajabu ajabu sina ustaarabu nayo. Ninachotaka ni wananchi wanufaike na dawa zinazotolewa na Serikali,” alisisitiza.

Dkt. Mwigulu amesema Serikali ya Awamu ya Sita inaendelea kuboresha huduma za afya nchini kwa kuongeza bajeti ya dawa, vifaa tiba pamoja na miundombinu ya hospitali ili wananchi wapate huduma bora karibu na maeneo yao.

Aidha, amewataka watumishi wa sekta ya afya kufanya kazi kwa uadilifu na kuwahudumia wananchi kwa haki bila kuwapa usumbufu usio wa lazima, akisisitiza kuwa fedha zinazotolewa na Serikali zinapaswa kuonekana moja kwa moja katika huduma wanazopata wananchi.

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo wilayani Kilolo, mkoani Iringa, alipokuwa akizungumza na wananchi katika moja ya ziara yake ya kikazi mkoani humo, ambapo alipokea na kusikiliza changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi katika sekta mbalimballina huduma za kijamii.


Na Mwandishi Wetu, Michuzi TV

TANZANIA inatarajiwa kupokea ujumbe wa viongozi wa elimu ya juu kutoka Malaysia, wakiwemo maofisa kutoka Wizara ya Elimu ya Malaysia, Education Malaysia Global Services (EMGS) pamoja na wawakilishi wa vyuo vikuu tisa watakaoshiriki Maonesho ya Elimu ya Malaysia yatakayofanyika Juni 1–3, 2026 katika Hoteli ya Serena, Dar es Salaam.

Maonesho hayo yanayoratibiwa kwa ushirikiano wa Global Education Link (GEL) na wadau wa elimu kutoka Malaysia yanalenga kufungua fursa za udahili, ufadhili wa masomo, ushirikiano wa kitaaluma pamoja na kuimarisha mahusiano ya elimu kati ya Tanzania na Malaysia.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa Global Education Link, Abdumalik Mollel, alisema ujio huo ni wa kimkakati kwa kuwa unaleta pamoja mamlaka muhimu za elimu ya juu, vyuo vikuu na taasisi zinazoratibu wanafunzi wa kimataifa.

Alisema vyuo vitakavyoshiriki vitatoa taarifa kuhusu programu za masomo, gharama za elimu, mazingira ya kujifunzia, taratibu za udahili pamoja na nafasi za ufadhili wa masomo kwa wanafunzi wa Tanzania.

“Hii siyo maonesho ya kawaida ya udahili pekee. Ni fursa ya kuunganisha Tanzania na Malaysia katika elimu ya juu, scholarship, tafiti, ubunifu na ushirikiano wa kitaaluma,” alisema Mollel.

Miongoni mwa vyuo vinavyotarajiwa kushiriki ni Asia Pacific University of Technology and Innovation (APU), University of Malaya, University Putra Malaysia (UPM), University Kebangsaan Malaysia (UKM), UCSI University, University Kuala Lumpur, University Selangor (UNISEL) na Putra Business School.

Mollel alisema maonesho hayo pia yatafungua fursa za ushirikiano kati ya vyuo vya Tanzania na Malaysia kupitia makubaliano ya ushirikiano (MoU), tafiti za pamoja, ubadilishanaji wa wanafunzi na wahadhiri pamoja na programu za kitaaluma na ubunifu.

Alisema maonesho hayo yanatoa fursa muhimu kwa wanafunzi, wazazi, taasisi za elimu na Serikali katika kujenga mahusiano ya kimataifa na kuongeza nafasi za elimu kwa vijana wa Tanzania.


Katika mwendelezo wa kuimarisha utimamu wa mwili na akili, Benki ya CRDB imeendeleza programu yake ya Wellness Day inayolenga kuwapa wafanyakazi nafasi ya kujali afya zao kwa kuwa na uwiano kati ya majukumu ya kiofisi na maisha binafsi Jijini Bunjumbura - Burundi.

Kupitia Wellnes Day inayoadhimishwa tangu mwaka 2021, wafanyakazi wa Benki ya CRDB hupata mafunzo na semina juu ya siha ya mwili, lishe bora pamoja na ustawi wa akili.

Akizungumza katika programu hiyo ilyofanyika viwanja vya Serenity Garden (Avenue du Large) ambako wafanyakazi walikuwa wanafanya mazoezi ya aina tofauti pamoja na kushiriki michezo sambamba na kupima afya. Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Benki Burundi, Fredric Siwale mara baada ya kuwaongoza katika mazoezi ya viongo, alisema mfanyakazi anapokuwa na afya njema na saikolojia yake ikakaa sawa basi atakuwa na uwezo mkubwa wa kutimiza majukumu yake na kuwahudumia wateja kwa viwango vinavyokubalika.

“Wakati wote Benki yetu imekuwa mstari wa mbele katika kuwajali sana wateja na wadau wetu. Wakati wote tunalenga kuwapa huduma bora lakini tunafahamu hatuwezi kufanikisha hilo bila kuwa na wafanyakazi wenye utulivu wa mwili na akili, hii ndio maana ya kuwa Benki kiongozi ambapo kwa mwaka huu Benki imetunukiwa tuzo ya Mwajiri bora "Top Employer" aliongeza Siwale.

Wellness Day ni mkakati wa Benki yetu ya CRDB kutoa fursa kwa wafanyakazi kupima afya, kupata ushauri wa vyakula vya kutumia pamoja na utatuzi wa changamoto nyingine yoyote inayoweza kupunguza ufanisi wa mfanyakazi,” aliongeza Siwale.

Huu ni mwendelezo wa programu hiyo ambayo kwa mwaka huu ilizinduliwa jijini Mwanza, baadae kufanyika kanda ya Kasikazini, Kusini, Magharibi na sasa imefanyika Burundi lengo ni kuwafikia wafanyakazi wote katika kanda zote nane za Benki ya CRDB pamoja na nje ya nchi ambako benki inatoa huduma kuhakikisha wafanyakazi wote wa taasisi hii kubwa zaidi ya fedha nchini inakuwa na wafanyakazi wenye weledi na wanaotoa huduma za kiwango cha juu.

Akieleza jinsi walivyojipanga kufikisha programu hiyo kwa kila mfanyakazi, Kaimu Mkurugenzi Rasiliamali watu wa Benki ya CRDB, Timoth Fasha amesema wataalamu wa afya wanashauri juu ya kupata usingizi wa kutosha, kufanya mazoezi ya mwili, kupata lishe bora pamoja na ushauri juu ya afya ya akili hivyo ni muhimu kwa kila mfanyakazi kuyafahamu mambo haya na kuyaishi.

“Mfanyakazi anaweza akajisahau kuijali afya yake kutokana na sababu mbalimbali za majukumu ya kikazi. Hivo kupitia Programu ya Wellness Day, tunawakumbusha wafanyakazi wetu umuhimu wa kuwa na ratiba ya kuulinda mwili kwa vipimo vya kitabibu, mazoezi pamoja na ushauri wa kitaalamu. Hii ni muhimu kwa sababu mafanikio ya Benki ya CRDB yanatokana na mchango wa kila mmoja wetu hivyo ni muhimu kuwa na afya njema ili kuendeleza ubora huo kwa wateja wetu,” amesema Fasha.

Kutokana na wingi wa majukumu, mfanyakazi anaweza kujikuta anatumia muda mwingi kukaa ofisini hivyo kutofanya mazoezi ya mwili au kuzungumza na watu wengine hali ambayo ikidumu kwa muda mrefu inaweza kusababisha msongo wa mawazo iwapo kutatokea hata changamoto ndogo tu kwa mhusika.

Kupitia Wellness Day, wafanyakazi wa Benki ya CRDB wanapata fursa ya kushiriki michezo ya aina tofauti, mazoezi ya viungo pamoja na kukutana na madaktari na washauri nasaha wanaotoa elimu ya saikolojia, mahusiano, matibabu, msongo wa mawazo, pamoja na lishe na usimamizi wa mtindo wa maisha.




Benki ya NMB imesema itaendelea kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar pamoja na taasisi zake katika kuimarisha mifumo ya malipo, makusanyo, huduma za kidijitali na suluhisho za kifedha zinazolenga kuongeza ufanisi wa huduma kwa wananchi na wawekezaji.

Kauli hiyo imetolewa wakati wa Mkutano wa Watendaji Wakuu na Wenyeviti wa Bodi wa Taasisi za Kizanzibari unaofanyika Golden Tulip Airport Hotel, Zanzibar, kuanzia Mei 23 hadi 25, 2026, ambapo Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, aliwataka viongozi wa taasisi hizo kuleta mageuzi ya kiutendaji yatakayoongeza tija, kupunguza utegemezi kwa Serikali Kuu na kuwezesha taasisi kutoa gawio kwa Serikali.

Akifungua mkutano huo, Rais Dkt. Mwinyi alisema kasi ya maendeleo itaongezeka zaidi kupitia ushirikiano imara na sekta binafsi, akitolea mfano mabenki yanayofanya vizuri nchini kwa kuonyesha ukuaji mkubwa, faida nzuri na kutoa gawio kubwa kwa Serikali.

 “Taasisi zetu zinapaswa kujifunza kutoka kwenye mifano mizuri ya sekta binafsi, hasa mabenki binafsi yanayoonyesha ufanisi, faida na mchango mkubwa wa gawio kwa Serikali,” alisema Dkt. Mwinyi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Biashara za Serikali wa NMB, Bi. Vicky Bishubo, alisema NMB inaona Zanzibar kama mshirika muhimu katika ajenda ya maendeleo kupitia uwekezaji, uchumi wa bluu, utalii, biashara, teknolojia na huduma za kifedha. Alisema NMB tayari inashirikiana na EGAZ, ZIPA na taasisi nyingine za Zanzibar katika kuboresha huduma za kidijitali, uwekezaji na uhifadhi wa maeneo ya kimkakati, huku pia ikitoa mafunzo kwa zaidi ya wajasiriamali 10,000 wa Zanzibar wanaojihusisha na mwani, chumvi na uvuvi.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, akipokea zawadi maalum kutoka kwa Meneja wa Biashara Zanzibar wa Benki ya NMB, Bi. Naima Said Shaame, wakati wa Mkutano wa Watendaji Wakuu na Wenyeviti wa Bodi wa Taasisi za Kizanzibari uliofanyika Golden Tulip Airport Hotel, Zanzibar. Kushoto ni Mkuu wa Idara ya Biashara za Serikali wa NMB, Bi. Vicky Bishubo. Zawadi hiyo ilitolewa kama ishara ya kuthamini uongozi wa Rais Dkt. Mwinyi katika kukuza uchumi wa Zanzibar na kuimarisha mazingira wezeshi kwa biashara na uwekezaji.









Top News