OFISA Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) CPA. Nicodemus Mkama amesema mafanikio ya asilimia 760.78, yameifanya Hatifungani ya iTrust kuweka historia ya kuwa Hatifungani iliyopata mafanikio makubwa zaidi kupita hatifungani zote zilizowahi kutolewa hapa nchini. 

Amesema hatifungani iliyokuwa inashikilia rekodi hiyo, ni Hatifungani ya kampuni ya First Housing Finance Limited yaani MAKAZI Bond ambayo ilipata mafanikio ya asilimia 661.1 na kuorodheshwa kwenye Soko la Hisa tarehe 09 Juni 2026 huku akiipongeza iTrust kwa kuvunja rekodi na kuendelea kuweka rekodi za mafanikio katika masoko ya mitaji.

CPA.Mkama ameyasema hayo leo Julai 8,2026 jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya kuorodheshwa kwa Hatifungani ya Kampuni ya iTRUST Finance Limited katika Soka la Hisa Dar es Salaam 

“Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) pamoja na wadau wote wa sekta ya masoko ya mitaji tumefurahishwa sana na hatua hii, na tunatoa pongezi za dhati kwa Bodi na Menejimenti ya iTrust Finance Limited, wataalamu wote waliohusika kwa kuweka rekodi hii ya kihistoria.”

Amesema iTrust Finance Limited imeendelea kuwa mfano bora na wa kuigwa kwa kampuni na taasisi katika sekta ya umma na binafsi, kwani kampuni hiyo imekuwa ikitumia vizuri fursa zinazopatikana katika masoko ya mitaji kupata rasilimali fedha za kukuza na kuendeleza biashara; kuimarisha utendaji wa Kampuni; na kugharamia shughuli za maendeleo.

“Tangu mwaka 2021 (wakati huo kampuni hii ikitumia jina la Imaan Finance Limited) na hadi hivi sasa ikiwa na jina la iTrust Finance Limited, Kampuni hii imetumia fursa za masoko ya mitaji kwa njia ya utoaji wa Hatifungani, Sukuk na Mifuko ya Uwekezaji wa Pamoja.

Akifafanua zaidi amesema hatifungani hiyo ni ya kipekee na muhimu katika maendeleo na ustawi wa masoko ya mitaji, sio tu Tanzania, bali katika ukanda wa Afrika Mashariki, kwani hatifungani hii inaweka historia na rekodi kuu Tatu,

Amesema ni hatifungani ya kwanza (1) kuorodheshwa kwenye Soko la Hisa la Dar es Salaam, ikiwa imetolewa na kampuni yenye Leseni ya Uwakala wa Soko la Hisa (Licensed Broker/Dealer); na Leseni ya Usimamizi wa Mifuko ya Uwekezaji (Fund Manager) iliyotolewa na CMSA.

Pia ni hatifungani ambayo mauzo ya toleo la kwanza yameweza kuzidi kiasi cha Programu nzima ya Hatifungani yenye Thamani ya shilingi bilioni 100 zilizokuwa zitolewe katika awamu nne ndani ya miaka minne (bilioni 15, 20, 30 na 35, katika mwaka 2026, 2027, 2028 na 2029 mtawalia).

“Kama tulivyoshuhudia mauzo ya Hatifungani ya iTrust yamepata mafanikio ya asilimia 760.78, ambapo kiasi cha shilingi bilioni 114.12 kimepatikana, ikilinganishwa na shilingi bilioni 15 zilizotarajiwa,”amesema.

Akieleza zaidi amesema mojawapo ya malengo ya DIRA ya Taifa ya Maendeleo (DIRA 2050) ni kuona kuwa Sekta ya Fedha, inawezesha upatikanaji wa rasilimali fedha kwa ajili ya kukuza na kuendeleza biashara ambazo zinachangia ukuaji na ustawi wa sekta binafsi;

sekta ya umma na uchumi wa nchi kwa ujumla hapa nchini. 

“Hivyo basi, juhudi za iTrust Finance Limited zinatoa mchango katika utekelezaji wa malengo haya, na ni hatua madhubuti ya kuongeza fursa za uwekezaji katika masoko ya mitaji na kuleta matokeo chanya kwenye uchumi wa nchi yetu.”

Pia amesema kati ya wawekezaji waliowekeza kwenye hatifungani ya iTrust, asilimia 66.66 ni wawekezaji mmoja mmoja yaani Retail Investors na asilimia 33.34 ni Kampuni na Taasisi yaani Institutional investors . 

Aidha, asilimia 98.82 ni wawekezaji wa ndani na asilimia 1.18 ni wawekezaji wa kigeni huku akifafanua kuorodheshwa kwa hatifungani hiyo kunaongeza thamani ya uwekezaji katika Hatifungani za Kampuni na Taasisi kwa asilimia 5.46 na kufikia shilingi trilioni 2.20, kutoka shilingi trilioni 2.09. 

“Ushiriki mkubwa wa wawekezaji mmoja mmoja wa ndani ni hatua muhimu katika kuongeza ukwasi (liquidity) katika soko la hisa. Aidha, hii sehemu muhimu ya utekelezaji wa Mpango Jumuishi wa Huduma za Kifedha yaani National

Financial Inclusion Framework wenye lengo la kuongeza ushiriki wa wananchi kwenye sekta rasmi ya fedha.

“Takribani asilimia 89 ya maombi yote ya uwekezaji kwenye Hatifungani ya iTrust

yamefanyika na kupokelewa kupitia mifumo ya kidijitali, ambapo mfumo wa kidijitali wa iTrust App pekee umechangia zaidi ya asilimia 71 ya maombi yote.”

CPA.Mkama amesema mafanikio hayo ni uthibitisho wa imani ya waliyonayo wawekezaji kwa Kampuni ya iTrust Finance Limited na masoko ya mitaji nchini. Aidha, mafanikio hayo ni matokeo ya mazingira wezeshi ya kisera, kisheria na kiutendaji yanayotolewa na Serikali katika masoko ya mitaji. 




▪️Yaonesha nia ya kushirikiana na Serikali katika usafiri ya Mijini.

▪️Dkt. Mwigulu awahakikishia mazingira bora ya uwekezaji

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amekutana na Makamu wa Rais wa Kampuni ya ALSTOM ya nchini Ufaransa, Philippe Deller ambapo wamejadiliana kuhusu fursa za uwekezaji katika sekta ya miundombinu ya usafiri nchini Tanzania.

Katika mazungumzo hayo, Dkt. Mwigulu Nchemba aliikaribisha ALSTOM kuwekeza nchini, akieleza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wawekezaji na kutekeleza mageuzi yanayolenga kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha biashara, usafiri na uwekezaji katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Kwa Upande wake Bw. Phillepe alieleza nia ya kampuni hiyo kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya usafiri wa mijini.

Kampuni hiyo imeonesha utayari wa kuwekeza katika ujenzi wa mifumo ya usafiri wa haraka na miundombinu ya kisasa yenye lengo la kupunguza msongamano wa magari katika Jiji la Dar es Salaam, huku ikitazama pia fursa za utekelezaji wa miradi kama hiyo katika majiji ya Mwanza, Mbeya na Arusha.

Miradi hiyo inatarajiwa kuongeza ufanisi wa usafiri wa mijini, kupunguza muda wa safari, kuimarisha shughuli za biashara na uwekezaji, pamoja na kuchochea ukuaji wa uchumi na kuboresha maisha ya wananchi kupitia matumizi ya teknolojia za kisasa.

Mazungumzo hayo ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuimarisha ushirikiano na kampuni kubwa za kimataifa ili kuleta teknolojia, utaalamu na mitaji inayochochea maendeleo ya miundombinu na uchumi wa Taifa.

Kampuni ya ALSTOM, ina uzoefu mkubwa katika kubuni, kujenga na kuendesha mifumo ya kisasa ya usafiri wa umma ikiwemo reli za kisasa, treni za mwendo kasi, metro, tram na teknolojia za usimamizi wa usafiri.






-Ni kuanzia Agosti 12,Rais Samia na Rais Mwinyi kuongoza washiriki wakati wa tamasha

-Miradi ya maendeleo kuzinduliwa,fursa mbalimbali kuibuliwa


Na Said Mwishehe,Michuzi TV-Zanzibar

KIZIMKAZI Kumenoga! Hiyo ndio kauli mbiu iliyobeba Tamasha la Kizimkazi 20226 linatarajiwa kufanyika kuanzia Agosti 12 hadi Agosti 14 mwaka huu likiwa limesheheni fursa lukuki .

Katika tamasha hilo ambalo limejizoelea umaarufu mkubwa pia kutakuwa maonyesho, burudani na programu mbalimbali za kuvutia zinazolenga kutangaza utalii, uwekezaji na utamaduni wa Kizimkazi.

Akizungumza kuhusu maandalizi ya kuelekea tamasha hilo Wilaya ya Kusini Unguja visiwani Zanzibar leo Julai 8,2026 Mwenyekiti wa Kamati ya Tamasha la Kizimkazi Mahfodh Said Omar amesema katika tamasha hilo miradi mbalimbali ya maendeleo itazinduliwa.

Katika uzinduzi wa tamasha la Kizimkazi litafunguliwa rasmi na Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Dk.Ali Hussein Mwinyi na kisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Samia Suluhu Hassan atakuwa mgeni katika siku ya kufunga tamasha hilo.

“Tunawaalika wawekezaji, wadau wa mandeleo, wafanyabiashara, wadau wa utalii na wananchi kwa ujumla kushiriki Kizimkazi Festival 2026, kwani mwaka huu tamasha limenoga na limebeba fursa nyingi kwa wote.

“Leo tunazindua rasmi maandalizi ya Kizimkazi Festival 2026. Tamasha hili lilianzishwa na wazee pamoja na wananchi wa Kizimkazi kwa lengo la kuhifadhi na kuenzi utamaduni, mila na desturi za eneo letu. Kadiri miaka ilivyopita, tamasha limeendelea kukua na sasa limekuwa jukwaa muhimu la kutangaza utalii,uwekezaji na mendeleo ya jamii.

“Kizimkazi Festival ni tamasha la wananchi wa Kizimkazi. Dhamira yake ni kuitangaza Kizimkazi kama eneo lenye historia, utamaduni, vivutio vya utalii na fursa nyingi za uwekezaji kwa manufaa ya Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ujumla.”

Kuhusu malengo ya Tamasha la Kizimkazi amesema ni kutangaza fursa za uwekezaji, kutangaza vivutio vya utalii pamoja na kuhifadhi na kuenzi utamaduni wa Kizimkazi.

Wakati kwa upande wa fursa za uwekezaji ni Utalii na hoteli, Uchumi wa Buluu, Uvuvi, Biashara na huduma mbalimbali, pamoja na miradi mingine ya mandeleo.

Akizungumzia miradi itakayozinduliwa wakati wa tamasha la Kizimkazi ni uzinduzi wa mradi wa maji Kizimkazi, uzinduzi wa kiwanja cha watoto Kibu Teni,ufunguzi wa nyumba za kuishi Bopar Enterprises, Jiwe la msingi Salaam Cane Restaurant-K/Dimbani.

Miradi mingine itakayozinduliwa ni mradi wa mabweni mapya -Hasnu Makame Sekondari-Kibuteni ,jiwe la msingi jengo la maendeleo Kibuteni na uzinduzi wa hoteli la kitalii ya Johari-K Mkunguni.

Akielezea zaidi amesema pia kupitia tamasha hilo wanatangaza fursa za uwekezaji, vivutio vya utalii pamoja na kuhifadhi na kuenzi utamaduni wa Kizimkazi.

Ametumia nafasi hiyo kuelezea kupitia tamasha hilo manufaa yanayopatikana ni kuvutia uwekezaji, kuongeza watalii, ajira, biashara, mapato ya wananchi na Serikali, na kuchangia uchumi wa Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

“Tunawakaribisha wawekezaji, wadau wa utalii, tour operators, tour guides, travel agencies, wadhamini, vyombo vya habari, wasanii, watu mashuhuri na wadau wa maendeleo kushiriki Kizimkazi Festival ili kujionea fursa na kushiriki kuitangaza Kizimkazi duniani.”

Mwenyekiti huyo wa maandalizi tamasha la Kizimkazi amesema ujumbe mkuu katika tamasha hilo inasema Kizimkazi Festival si tamasha la burudani pekee; ni jukwaa la maendeleo linalounganisha utamaduni, utalii na uwekezaji kwa manufaa ya Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

“Karibuni Kizimkazi Festival mshuhudie utajiri wa utamaduni wetu, mjionee fursa za uwekezaji na vivutio vya utalii, na muwe sehemu ya safari ya kuijenga Kizimkazi kuwa kitovu cha maendeleo.”




Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma, Alimwoni Chaula amepongeza ushiriki wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba, 2026 akieleza kuwa maonesho hayo ni jukwaa muhimu la kulitangaza jiji na fursa zake kwa wananchi na wawekezaji.

Alitoa pongezi hizo alipotembelea banda la Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwenye maonesho hayo yanayoendelea jijini Dar es Salaam, ambapo alipata nafasi ya kuelezwa huduma zinazotolewa, maeneo ya uwekezaji pamoja na fursa mbalimbali zinazopatikana ndani ya Jiji la Dodoma.

Chaula alisema kuwa ameridhishwa na ushiriki wa jiji katika maonesho hayo na kusisitiza umuhimu wa kutumia kikamilifu nafasi hiyo kujitangaza ili wananchi wanaotembelea banda hilo waweze kufahamu na kuvutiwa na fursa zilizopo ndani ya Jiji la Dodoma.

"Ni vizuri mkatumia maonesho haya kujitangaza kikamilifu, kueleza kwa uwazi huduma mnazotoa, maeneo ya uwekezaji na fursa mbalimbali zilizopo ndani ya jiji letu ili wananchi na wadau wanaotembelea banda hili waone umuhimu wa kuchangamkia fursa hizo" alisema Chaula.

Aidha, alisisitiza kuwa ushiriki wa Jiji la Dodoma katika Maonesho ya Sabasaba unapaswa kuwa chachu ya kuhamasisha uwekezaji, kukuza biashara na kutangaza vivutio pamoja na huduma zinazotolewa na halmashauri kwa lengo la kuchochea maendeleo ya kiuchumi ya jiji hilo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Jiji la Dodoma, Dennis Gondwe alisema kuwa ushiriki wa jiji katika maonesho hayo unalenga kuitangaza Dodoma kama makao makuu ya nchi, kuonesha fursa za uwekezaji zilizopo, huduma za ardhi, biashara pamoja na miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa na halmashauri kwa manufaa ya wananchi na wawekezaji.

Maonesho ya 50 ya biashara ya Kimataifa Sabasaba, 2026 yanaendelea kuwa jukwaa muhimu kwa taasisi za umma na binafsi kuwasilisha huduma, bidhaa na fursa mbalimbali kwa wananchi huku yakitoa nafasi ya kubadilishana uzoefu na kuongeza uelewa kuhusu masuala ya maendeleo na uchumi.





Na John Mapepele, Wu hani - China

Serikali ya Tanzania imesisitiza dhamira yake ya kujenga sekta imara ya viwanda vya dawa na kuifanya nchi kuwa kitovu cha uzalishaji wa dawa kwa ukanda wa Afrika Mashariki na kwingineko barani Afrika, huku ikizidi kuvutia uwekezaji wa kimkakati kutoka China.

Akizungumza Julai 7,2026 katika kikao na viongozi wa kampuni ya Jointown Pharmaceutical Group nchini China, inayoongoza kwa uzalishaji wa madawa kwa upande wa makampuni binafsi nchini hapa, Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa amesema Tanzania imejipanga kuendeleza Eneo Maalum la Kiuchumi la Dawa na Vifaa Tiba la Mloganzila, ambalo litakuwa kitovu cha uwekezaji katika uzalishaji wa dawa, malighafi za dawa (APIs) na vifaa tiba.

Amesema, eneo hilo limeboreshwa kwa miundombinu ya kisasa na linaunganishwa kwa urahisi na Bandari ya Dar es Salaam pamoja na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere.

Waziri Mchengerwa amebainisha kuwa Serikali iko tayari kushirikiana na Jointown katika kuanzisha uzalishaji wa malighafi za dawa, hatua itakayoongeza uwezo wa Tanzania kujitosheleza kwa dawa muhimu na kuiwezesha kuhudumia masoko ya kikanda.

“Ushirikiano kati ya Jointown na Bohari ya Dawa (MSD) unatarajiwa kuleta mageuzi katika mifumo ya ugavi, uhifadhi na usambazaji wa dawa nchini kupitia matumizi ya teknolojia na uzoefu wa kampuni hii kubwa hapa China katika usimamizi wa minyororo ya usambazaji duniani” amesema Mhe. Mchengerwa

Aidha Mhe. Mchengerwa amethibitisha Serikali inayoongozwa na Rais wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, inafuatilia kwa karibu uwekezaji wa dawa nchini na ameahidi ushirikiano wa Serikali kwa wawekezaji watakaochangia maendeleo ya sekta ya afya.

Katika kuonesha utayari wa Serikali, Waziri Mchengerwa amesema Tanzania ipo tayari kutenga maeneo ya kutosha kwa ajili ya uwekezaji wa uzalishaji wa malighafi za dawa, akieleza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya dhamira ya dhati ya kuharakisha uanzishwaji wa viwanda vya kisasa vitakavyozalisha dawa kwa matumizi ya ndani na kwa ajili ya soko la Afrika.







Na Mwandishi Wetu
KAMPUNI ya NIC Insurance imewahimiza wamiliki wa vyombo vya moto nchini kuhakikisha wanakata bima ili kujikinga na athari za kifedha zinazoweza kujitokeza pindi yanapotokea majanga au ajali.

Wito huo umetolewa na Afisa Bima wa NIC Insurance, Iman Mollel, wakati akizungumza na waandishi wa habari katika Banda la kampuni hiyo kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere jijini Dar es Salaam.

Mollel amesema NIC Insurance imeendelea kuboresha utoaji wa huduma kwa kuhakikisha madai ya fidia kwa magari yaliyoharibika kiasi cha kutotengenezeka (total loss) yanashughulikiwa kwa haraka, ambapo malipo hufanyika ndani ya siku saba baada ya mteja kukamilisha nyaraka zote zinazohitajika.

Amesema kampuni hiyo inatoa bima kwa aina mbalimbali za vyombo vya moto, ikiwemo magari binafsi, magari ya biashara, magari ya mizigo, mabasi na magari ya abiria, bajaji pamoja na pikipiki, ili kuhakikisha wamiliki wake wanapata kinga dhidi ya hasara zinazoweza kujitokeza.

Aidha, Mollel amesema NIC Insurance imeweka huduma za kidijitali zinazowawezesha wateja kupata huduma za bima kwa njia ya mtandao, hatua inayolenga kupunguza gharama na muda wa kusafiri kufuata huduma katika ofisi za kampuni hiyo.

Ametoa wito kwa wananchi wanaotembelea Maonesho ya Sabasaba kufika katika banda la NIC Insurance ili kupata elimu kuhusu huduma mbalimbali za bima pamoja na ushauri wa kitaalamu utakaowasaidia kuchagua bima zinazokidhi mahitaji yao.






Na Mwandishi Wetu
MAMLAKA ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), kupitia Chuo cha VETA Chang'ombe, imebuni pikipiki ya magurudumu matatu (Bajaj) yenye teknolojia ya kisasa ya kufagia barabara, ubunifu unaolenga kuongeza ufanisi katika usafi wa miji na kupunguza gharama za usafi wa mazingira.

Akizungumza katika Banda la VETA kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere jijini Dar es Salaam, Mwalimu wa Chuo cha VETA Chang'ombe, Emmanuel Bukuku, amesema kifaa hicho kina uwezo wa kufagia barabara urefu wa kilomita mbili kwa saa moja.

Bukuku amesema mashine hiyo imeundwa kwa mfumo unaokusanya vumbi, mchanga na taka ndogondogo wakati wa kufagia na kuzipeleka kwenye sehemu maalumu ya kuhifadhi, hivyo kuacha barabara zikiwa safi na salama kwa matumizi.

Ameeleza kuwa ubunifu huo unaweza kuwa suluhisho kwa halmashauri, manispaa na majiji nchini katika kuboresha huduma za usafi wa barabara kwa kutumia teknolojia ya ndani, badala ya kutegemea nguvu kazi kubwa ya watu pekee.

"Teknolojia hii imeundwa na wataalamu wetu wa VETA kwa kuzingatia mahitaji ya mazingira ya Tanzania. Inaongeza ufanisi, inapunguza muda wa kufanya usafi na inaweza kusaidia kupunguza gharama za uendeshaji wa shughuli za usafi katika mamlaka za serikali za mitaa," amesema Bukuku.

Aidha, amesema Chuo cha VETA Chang'ombe kipo tayari kupokea maombi kutoka kwa taasisi za umma na binafsi kwa ajili ya kutengeneza vifaa hivyo kulingana na idadi na mahitaji ya mteja, hatua inayolenga kuendeleza matumizi ya teknolojia za ubunifu zinazotengenezwa nchini.
Mkutano Mkuu wa Kwanza wa Baraza la Mawaziri wa Masuala ya Kijamii wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) umehitimishwa Julai 7, 2026 jijini Dar es Salaam, kwa kusainiwa kwa ripoti maalumu inayohusu uwekaji wa sera na mikakati thabiti katika sekta za jinsia, watoto, vijana, wazee, hifadhi ya jamii, kazi, ajira na uhamiaji.

Mawaziri kutoka nchi zote 8 wanachama wa EAC wameidhinisha na kusaini ripoti hiyo ili ianze kutekelezwa kikanda, ikilenga kuhakikisha kuwa faida za mtangamano wa kiuchumi na kijamii zinamfikia kila mwananchi kwa usawa, baada ya kupitia mapendekezo yaliyowasilishwa na wataalamu na Makatibu Wakuu.

Mkutano huo wa kihistoria uliongozwa na Naibu Waziri Mkuu wa Kwanza na Waziri anayeshughulikia Ushirikiano wa Afrika Mashariki wa Uganda, Mhe. Rebecca Kadaga, ambaye aliongoza zoezi la utiaji saini wa ripoti hiyo kwa kushirikiana na Mawaziri wenzake wa ukanda huo.

Ujumbe wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika mkutano huo uliongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Maendeleo ya Vijana) Mhe. Joel Nanauka, akiambatana na Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu, Mhe. Maryprisca Mahundi, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Mhe. Dkt. Eveline Munisi, pamoja na Makatibu Wakuu, wataalam wa wizara husika, na wa mifuko ya hifadhi ya jamii nchini.

Katika majadiliano hayo, viongozi hao walisisitiza kuwa utekelezaji wa sera hizi utaleta mageuzi makubwa na ya kihistoria katika mifumo ya ajira, ulinzi wa jamii, ustawi wa makundi maalum, pamoja na usimamizi madhubuti wa masuala ya uhamiaji katika ukanda mzima.

Kuhitimishwa kwa mkutano huo na kusainiwa kwa ripoti hii ya pamoja kunadhihirisha dhamira thabiti ya EAC katika kujenga ukanda wenye sera shirikishi, maendeleo jumuishi, na ustawi endelevu kwa wananchi wake.












Na Mwandishi Wetu
MAMLAKA ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) imewahimiza Watanzania kushiriki kikamilifu katika mapambano dhidi ya dawa duni na zisizo salama, ikisisitiza kuwa ulinzi wa afya ya jamii ni jukumu la kila mwananchi.

Hayo ameyasema Meneja wa Mawasiliano na Elimu kwa Umma wa TMDA, Gaudensia Simwanza, alipokuwa akitoa elimu kwa wananchi waliotembelea banda la TMDA katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere jijini Dar es Salaam.

Simwanza amesema dawa duni na zisizosajiliwa mara nyingi huingizwa nchini kwa njia zisizo rasmi, hivyo wananchi wanapaswa kuwa macho na kutoa taarifa mara wanapobaini bidhaa zinazotiliwa shaka badala ya kuzifumbia macho.

Ameeleza kuwa matumizi ya dawa duni yanaweza kusababisha madhara makubwa kwa afya ya watumiaji na kuhatarisha maisha ya wananchi, jambo linaloweza kuathiri nguvu kazi na maendeleo ya taifa.

Aidha, amewataka wananchi kujenga utamaduni wa kukagua tarehe za mwisho wa matumizi wa dawa kabla ya kuzinunua au kuzitumia. Amesema endapo watabaini dawa zilizokwisha muda wake wa matumizi au zinazoshukiwa kuwa duni, wanapaswa kutoa taarifa TMDA ili zichukuliwe hatua za kuziondoa sokoni.

Gaudensia amesisitiza kuwa dawa duni hazina nafasi katika soko la Tanzania, akibainisha kuwa mafanikio ya kuzuia bidhaa hizo yanategemea ushirikiano wa karibu kati ya TMDA na wananchi katika kulinda afya ya jamii.

📍 Aielekeza kuboresha mikakati ya kudhibiti migongano kati ya wanyamapori na binadamu

Na Beatus Maganja, Morogoro

Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb.) ameipongeza Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) kwa mafanikio yake katika kuvutia wawekezaji jambo lililotajwa kuchangia ongezeko la mapato ya Taasisi hiyo, huku akiielekeza Menejimenti ya mamlaka hiyo kuandaa mikakati ya muda mfupi, ya kati na ya muda mrefu ya kudhibiti migongano baina ya wanyamapori na binadamu.

Akizungumza na Bodi ya Wakurugenzi na Menejimenti ya TAWA alipofanya ziara ya kikazi katika Ofisi za Makao Makuu ya TAWA mkoani Morogoro Julai 7, 2026, Dkt. Kijaji alisema mwaka mpya wa fedha unapaswa kuwa mwanzo wa utekelezaji wenye matokeo makubwa katika kuimarisha uhifadhi wa maliasili na kuongeza kasi ya kudhibiti migongano kati ya binadamu na wanyamapori ili kuhakikisha usalama wa wananchi na wanyamapori kwa pamoja.

"Tunapaswa kuwa na mikakati ya muda mfupi, wa kati na mrefu itakayowezesha kupunguza migongano kati ya wanyamapori na binadamu. Lengo letu ni kuona wananchi wanakuwa salama na wanyamapori wanaendelea kuhifadhiwa" alisema Dkt. Kijaji.

Aidha, Waziri huyo aliielekeza TAWA kuendelea kuimarisha ushirikiano na wananchi wanaozunguka maeneo ya hifadhi, akisisitiza kuwa wananchi ndiyo walinzi namba moja wa rasilimali za wanyamapori. Pia alisisitiza kuimarishwa kwa ulinzi wa maeneo ya hifadhi kwa kutoruhusu shughuli za kibinadamu ndani ya maeneo hayo, ikiwemo uvamizi kwa ajili ya kilimo na matumizi mengine yasiyoruhusiwa kisheria.

 Vilevile Mheshimiwa Waziri Kijaji aliipongeza TAWA kwa usimamizi mzuri wa fedha za Serikali hususan katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo pamoja na matumizi ya teknolojia katika shughuli mbalimbali za uhifadhi.

Awali akiwasilisha taarifa ya utendaji wa Bodi ya Wakurugenzi wa TAWA, Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Mej. Jen. (Mstaafu) Hamis R. Semfuko, alisema kuimarika kwa ulinzi na usimamizi wa rasilimali za wanyamapori kumechangia ongezeko la idadi ya wanyamapori katika maeneo yanayosimamiwa na mamlaka hiyo. Alisema kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2025, idadi ya swala aina ya Puku imeongezeka kutoka 1,950 mwaka 2021 hadi 3,185 mwaka 2025, sawa na ongezeko la asilimia 63. Aidha, kaya 1,107 zilizokuwa katika Kijiji cha Ngombo, Wilaya ya Malinyi zimehama kutoka ndani ya Pori la Akiba Kilombero kufuatia utatuzi wa migogoro ya matumizi ya ardhi.

Semfuko alisema TAWA pia imeendelea kuimarisha uwekezaji baada ya kusaini mikataba mitatu ya uwekezaji mahiri na kufikisha jumla ya maeneo 16 ya uwekezaji huo, ambao kwa sasa unachangia asilimia 46 ya mapato ya mamlaka. Vilevile, idadi ya watalii wa picha imeongezeka na kufikia 267,575 ikilinganishwa na watalii 240,967 waliotembelea maeneo yanayosimamiwa na TAWA katika mwaka wa fedha 2024/25.

Aliongeza kuwa TAWA imeimarisha mwitikio wa matukio ya wanyamapori wakali na waharibifu kwa kukamilisha ujenzi wa mabwawa 14, vizimba 31 na vituo 14 vya askari, hatua iliyochangia kuokoa maisha ya wananchi na mali zao.

 Aidha, gawio la shilingi bilioni 9.7 limetolewa kwa WMA 16, vijiji 161 na Halmashauri za Wilaya 41, huku maelfu ya wananchi wakiendelea kunufaika na shughuli za uvuvi na ufugaji nyuki katika maeneo ya hifadhi. Kwa upande wa utendaji wa taasisi, alisema TAWA pia imeajiri watumishi 661 kuongeza nguvu kazi na kufikia makusanyo ya shilingi bilioni 92.28 hadi Juni 2026, ikilinganishwa na shilingi bilioni 87.32 zilizokusanywa mwaka uliotangulia.

Katika ziara hiyo, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb.) aliambatana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi, pamoja na Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Wizara, Bw. Bernard Marcelline. Ziara hiyo imeendelea kudhihirisha dhamira ya Serikali ya kuimarisha usimamizi wa rasilimali za wanyamapori ili kuleta manufaa kwa wananchi, sambamba na kutafuta mwarobaini wa kukabiliana na changamoto za migongano baina ya wanyamapori na binadamu.










Top News