Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Mzumbe, Prof. William Mwegoha, ameongoza kikao maalumu cha maprofesa wa chuo hicho  kikilenga kujadili mbinu za kuimarisha utafiti, ushauri wa kitaaluma pamoja na mchango wa chuo katika maendeleo ya jamii.

Akihutubia kikao hicho, Prof. Mwegoha ambaye pia alikuwa Mwenyekiti wa jukwaa hilo, alisisitiza umuhimu wa kujenga mshikamano miongoni mwa maprofesa na kutumia mafanikio yaliyopo kama chachu ya maendeleo zaidi. Alieleza kuwa jukwaa hilo limekusudiwa kuunda mazingira ya majadiliano ya wazi yatakayosaidia kutathmini mafanikio yaliyopatikana, sambamba na kuweka dira ya pamoja ya maendeleo ya baadaye akisisitiza umuhimu wa kuongeza vyanzo vya mapato ya ndani ya chuo kupitia shughuli za utafiti na ushauri elekezi. 

Kwa upande wake, Naibu Makamu Mkuu wa Chuo – Taaluma, Utafiti na Ushauri, Prof. Hawa Tundui, alieleza kuwa jukwaa hilo ni hatua muhimu katika kujenga utamaduni thabiti wa kitaaluma. Alibainisha kuwa chuo kina maprofesa kamili watano, maprofesa washiriki 29, wahadhiri waandamizi 64 na wahadhiri 62, huku wahadhiri wasaidizi na wasaidizi wa kufundisha wakizidi 300, hali inayoonesha msingi mpana wa kukuza wanataaluma wa baadaye. Aidha, alisisitiza umuhimu wa uanagenzi katika kuwalea wanataaluma chipukizi kwa weledi.

"Maprofesa wanapaswa kuwa vinara wa mabadiliko kwa kuongoza katika uandishi wa kitaaluma, usimamizi wa tafiti na matumizi ya matokeo ya tafiti katika kutatua changamoto za kijamii".Alisisitiza Prof. Tundui

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Utafiti, Machapisho na Masomo ya Uzamili, Dkt. Nsubili Isaga, alieleza kuwa jukwaa hilo litaimarisha maeneo muhimu ikiwemo uanagenzi (Mentorship),utafutaji wa rasilimali kupitia miradi ya utafiti na ushauri, pamoja na kuendeleza huduma kwa jamii. Aidha, alibainisha kuwa jukwaa hilo sasa litakuwa likifanyika kila mwaka kama sehemu ya utamaduni wa chuo wa kujipima na kupanga maendeleo ya baadaye.

Katika hatua nyingine mtoa mada Mwalikwa katika jukwaa hilo ambaye pia ni Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Mzumbe mstaafu, Prof. Joseph Kuzilwa, alisisitiza kuwa uanagenzi ni jukumu la msingi la uprofesa linalolenga kukuza kizazi kijacho cha wasomi. Alieleza kuwa uanagenzi bora unahitaji mwongozo wa karibu, kushirikishana uzoefu na mifumo imara ya kuwajengea uwezo wanataaluma chipukizi kitaaluma, kwa vitendo na kimaadili.

Aidha, alisisitiza kuwa maprofesa wanapaswa kuchukua nafasi ya kimkakati katika kusimamia na kuendeleza uanagenzi ili kuhakikisha ubora na uendelevu wa taaluma chuoni hapo.

Kupitia jukwaa hilo, msingi imara umewekwa wa kuimarisha mchango wa maprofesa katika utafiti, ubunifu na maendeleo ya chuo, sambamba na kuhakikisha kuwa maarifa yanayotolewa yanachangia moja kwa moja maendeleo ya jamii, chuo na taifa kwa ujumla. 


Makamu Mkuu wa Chuo Prof. William Mwegoha akihutubia katika kikao cha Maprofesa wa chuo kikuu Mzumbe cha kuweka mikakati ya kuongeza tafiti na kuchagiza Maendeleo ya Chuo.




WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Mei 1, 2026 amewasili mkoani Njombe kushiriki Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi).

Mgeni Rasmi katika maadhimisho hayo ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Kaulimbiu ya Maadhimisho hayo ni : “Kazi zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050”.






Na Mwandishi Wetu,Tabora

MAMLAKA ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) kwa kushirikiana na Wakala wa Huduma za Misitu (TFS) pamoja na kamati ya ulinzi na usalama mkoa wa Tabora, imefanya operesheni maalum katika hifadhi ya msitu wa Igombe river iliyopo wilaya ya Uyui na katika hifadhi ya msitu wa Nyahua iliyopo wilaya ya Skonge mkoani Tabora na kufanikiwa kuteketeza ekari 68 za mashamba ya bangi, kukamata gunia 133 za bangi huku watu saba (7) wakikamatwa katika operesheni hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Aprili  30 Aprili, 2026 katika ofisi za mkuu wa mkoa wa Tabora, Kamishna Jenerali Aretas Lyimo amesema, Mamlaka iko kwenye operesheni maalum ya kuteketeza dawa za kulevya zinazozalishwa nchini.

“Sasa hivi tuko kwenye kampeni maalum kuhakikisha kwamba tunateketeza dawa za kulevya zinazozalishwa nchini baada ya dawa za viwandani kupungua” amesema Lyimo.

Aidha, amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuiwezesha Mamlaka kuanzisha ofisi za DCEA kanda ya Magharibi yenye makao yake mkoani Tabora, hatua ambayo imeongeza ufanisi na kasi katika kudhibiti dawa za kulevya nchini.

Sambamba na hilo, Kamishna Jenerali Lyimo ameushukuru uongozi wa mkoa kwa kuunga mkono na kushiriki operesheni hiyo iliyofanikisha ukamataji na uteketezaji wa bangi zinazolimwa katikati ya mapori na hifadhi za taifa mkoani humo.

“Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya hatutakubali uhalifu huu uendelee. Tutahakikisha tunafanya operesheni endelevu katika maeneo yote na kuchukua hatua za makusudi kwa watu wanaolima na kuzalisha dawa za kulevya ndani na nje ya mapori” amesisitiza Lyimo.

Kwa upande wake mkuu wa mkoa wa Tabora Dkt. Paul Chacha, ameipongeza Mamlaka kwa kazi nzuri ya udhibiti wa dawa za kulevya inayoendelea mkoani humo na kuwaagiza askari wa TFS kuweka kambi katika mapori na maeneo ya hifadhi ili kumaliza kabisa tatizo la bangi katika mkoa wa Tabora.







Na Seif Mangwangi, Arusha 

BENKI ya CRDB, imepongeza taasisi ya Mawakili ya Wakili Welfare Mkoba kwa kupiga hatua kubwa ya uwekezaji hadi kufanikiwa kupata mtaji wa zaidi bilioni moja kwa kipindi kifupi tu cha miaka miwili tangu kuanzishwa kwake.

Aidha imeelezwa kuwa wastaafu wengi wamekuwa wakipoteza maisha kwa muda mfupi mara baada ya kustaafu kufuatia kukosa elimu sahihi ya fursa za kiuchumi zilizopo kwenye uwekezaji na kujikuta wakiwekeza kwenye maeneo yenye mazingira hatarishi ya kibiashara.

Hayo yameelezwa Aprili 29, 2026 Jijini hapa na Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Abdulmajid Nsekela katika salamu zake zilizowasilishwa na Kaimu Meneja wa Benki hiyo Kanda ya kaskazini, Emmanuel kafui wakati wa ufunguzi wa mkutano mkuu wa mwaka wa taasisi ya Mawakili ya Wakili Welfare Mkoba.

Kafui amesema waajiriwa wengi wamekuwa wakipata msongo wa mawazo pale wanapostaafu kufuatia kuwekeza kwenye maeneo yasiyokuwa sahihi na kuwataka kufanya utafiti kwanza kabla ya kujiingiza kwenye biashara pindi wanapostaafu.

Amesema Benki ya CRDB imeanzisha kitengo cha kutoa elimu ya uwekezaji pamoja na fursa za kiuchumi zilizopo na kuwakaribisha watanzania wote kufika kupata elimu hiyo ambayo ni Bure.

Awali akiwasilisha risala ya taasisi ya Wakili Welfare Mkoba, Mwenyekiti wa taasisi hiyo Wakili Laetitia Ntagazwa amesema taasisi hiyo ilianzishwa mwaka 2023 baada ya kubaini kuwepo kwa changamoto mbalimbali za kiuchumi na kijamii zinazowakabili Mawakili nchini.

Letiticia ambaye pia ni Kaimu Rais wa chama cha Mawakili Tanganyika (TLS), amesema tangu ilipoanzishwa taasisi hiyo yenye wanachama 350 wamefanikiwa kukusanya mtaji wa zaidi ya bilioni moja.

 " Kwa miaka miwili tangu tumeanzisha taasisi hii tumeshakusanya mtaji wa bilioni 1.350, ambapo pia tumewekeza kwenye mfuko wa uwekezaji wa UTT kiasi cha milioni400 na kutoa mikopo ya Milioni 840," amesema.

Amesema malengo ya taasisi hiyo Kwa mwaka 2026/2027 ni kukusanya kiasi cha bilioni 2, na kuendelea kutoa mikopo mingi zaidi Kwa Mawakili wanachama Ili kuwajenga kiuchumi na kufurahi maisha.

Letiticia amesema Kwa fedha walizokuwa nazo hivi sasa, Kila mwanachama ana uhakika wa kupata gawio la Milioni 200 Kwa mwaka jambo ambalo linaendelea kuleta faraja Kwa wanachama wake.

Aidha amewataka Mawakili zaidi kujiunga na taasisi hiyo kwa kile alichosema masharti ni rahisi sana na kwamba malengo ya taasisi ni kuwa na Benki yake inayojitegemea.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi hiyo, CPA Mfaume Mbuma amesema riba ya mkopo wa dharura ambayo wanachama hukatwa ni asilimia 3 huku riba ya mkopo mkubwa kuanzia milioni10 ikiwa ni asilimia 6 pekee.


Farida Mangube Morogoro 

Juhudi za kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi na changamoto za upatikanaji wa maji zimepata msukumo mpya kufuatia kuimarishwa kwa ushirikiano kati ya watafiti na jamii kupitia mradi wa kimataifa wa ICP Connect na Lab to Life.

Hatua hiyo imebainishwa wakati wa semina ya kuwasilisha matokeo ya awali ya tafiti za sayansi ya jamii iliyofanyika  Chuo Kikuu Mzumbe Kampas kuu Morogoro, ikiwa ni sehemu ya awamu ya pili ya mradi huo.

Mradi huo unatekelezwa kwa ushirikiano wa kimataifa unaojumuisha Chuo Kikuu cha Antwerp (Ubelgiji), Chuo Kikuu Mzumbe, Taasisi ya Sera ya Maendeleo (IOB), Chuo Kikuu cha Kikristo cha Uganda (UCU), pamoja na Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Afrika ya Nelson Mandela (NM-AIST), Arusha.

Akifungua semina hiyo, Kaimu Naibu Makamu Mkuu wa Chuo (Taaluma, Utafiti na Ushauri), Dkt. Proscovia Kamugisha, alisema mradi huo umeongeza uwezo wa kitaifa katika ufuatiliaji na tathmini ya maendeleo kupitia programu ya Shahada ya Uzamili ya Ufuatiliaji na Tathmini ya Maendeleo (MDME).

 Alisisitiza kuwa kuunganisha utafiti na jamii ni hatua muhimu katika kuhakikisha tafiti zinatoa matokeo yenye tija kwa maendeleo ya wananchi.

“Lengo letu ni kuhakikisha matokeo ya tafiti hayabaki kwenye makabrasha, bali yanawafikia na kuwasaidia wananchi moja kwa moja,” alisema Dkt. Kamugisha.

Kwa upande wake, Mratibu wa mradi huo, Dkt. Christina Shitima alieleza kuwa mafanikio makubwa ya mradi huo ni kuwashirikisha wananchi moja kwa moja katika tafiti. Alibainisha kuwa mbinu hiyo imeongeza uelewa wa pamoja kati ya watafiti na jamii, na kuwezesha kupatikana kwa suluhisho yanayokubalika na kudumu.

Naye Dkt. Lucy Massoi alisisitiza kuwa ushirikishwaji wa wadau unazifanya jamii kuwa sehemu ya suluhisho la changamoto zao wenyewe, hatua inayochangia kuboresha sera na kuinua ustawi wa maisha ya kila siku.

Akichangia mada katika semina hiyo, Bw. Richard Temu kutoka shirika la Twaweza alieleza kuwa matumizi ya mbinu za uraghbishaji (animation) yamekuwa chachu ya mabadiliko kwa jamii. Alifafanua kuwa mbinu hizo huwabadilisha wananchi kutoka kuwa wasikilizaji wa taarifa hadi kuwa washiriki hai katika kutambua na kutatua changamoto zinazowakabili.

“Wananchi wanapopewa nafasi ya kushiriki kikamilifu, wanakuwa sehemu ya suluhisho badala ya kuwa watazamaji,” alisisitiza.

Semina hiyo iliwakutanisha wadau mbalimbali wakiwemo wawakilishi kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero, Bodi ya Maji ya Bonde la Wami/Ruvu, TURUWASA Mvomero, viongozi wa kata na vijiji kutoka Tarafa ya Turiani, pamoja na watafiti, wanafunzi na wahadhiri kutoka taasisi washirika.

Katika uwasilishaji wa tafiti, wanafunzi walionesha matokeo ya kazi zao katika maeneo ya vijijini, yakitoa taswira halisi ya changamoto na suluhisho zinazotekelezeka. Katika kijiji cha Kilimanjaro, Kata ya Kisala, Tarafa ya Turiani, wilayani Mvomero, waliweka kifaa cha kisasa cha ufuatiliaji wa hali ya hewa kinachopima kasi ya upepo, unyevunyevu na mwenendo wa maji mtoni. Takwimu hizo zinasaidia kutoa tahadhari ya mapema dhidi ya mafuriko na kuongeza utayari wa jamii kukabiliana na majanga ya asili.

Katika kijiji cha Lusanga, utafiti uliofanywa ulibaini changamoto za muda mrefu za upatikanaji wa maji, ikiwemo utegemezi wa vyanzo visivyo salama, upungufu wa maji wakati wa kiangazi, pamoja na miundombinu duni. Ili kukabiliana na hali hiyo, watafiti walipendekeza kuimarishwa kwa usimamizi shirikishi wa rasilimali za maji, ulipaji wa huduma kwa wakati, na matumizi ya mbinu rahisi za usafi kama kuyachemsha au kuyachuja maji kabla ya matumizi.

Mbali na matokeo ya tafiti, semina hiyo ilionesha wazi kuwa kuunganisha maarifa ya kitaaluma na uzoefu wa jamii ni msingi muhimu wa kupata suluhisho endelevu kwa changamoto za maendeleo.

Akihitimisha semina hiyo, Kaimu Mkuu wa Idara ya Uchumi, Dkt. Robert Lihawa, alisema kuwa tafiti shirikishi zinapaswa kupewa kipaumbele kwani ndizo zenye uwezo wa kuleta mabadiliko ya kweli kwa jamii.

“Maendeleo endelevu hayawezi kufikiwa bila ushirikiano wa karibu kati ya watafiti, jamii na watunga sera,” alisema.

Kadri athari za mabadiliko ya tabianchi zinavyoendelea kuongezeka, jitihada kama hizi zinatarajiwa kuwa nguzo muhimu katika kusaidia jamii kujenga ustahimilivu na kuboresha upatikanaji wa rasilimali muhimu kama maji.







NMB Bank Plc has once again affirmed its leadership in workplace safety, employee wellbeing and organisational excellence after winning five accolades at the national AOSH Awards for the second consecutive year.

Held under the theme “A Good Psychosocial Working Environment: A Pathway to Thriving Workers and Stronger Organisations,” the awards recognised institutions that continue to create safer, healthier and more supportive workplaces.

NMB emerged as the winner of the Proactive Capital – Safety Investment Award, reflecting the Bank’s deliberate investment in workplace safety, risk prevention and employee protection. The Bank was also named First Runner-Up in Financial Administration for meritorious achievement in fiscal diligence and consistent administrative standards.

The Bank further received the First Runner-Up Inclusion & Support Award, while NMB Clock Tower Branch was named First Runner-Up in Financial Activities. NMB also secured Second Runner-Up recognition for outstanding commitment and support for employees with disabilities, underlining its continued focus on building a workplace where employees feel safe, included and empowered to thrive.













Na Mwandishi Wetu, Arusha

Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi, leo Aprili 30, 2026, “amewapiga msasa” waongoza watalii zaidi ya 230 wa kozi ya sita katika mfululizo wa mafunzo kwa wataalamu hao kuwaongezea uwezo zaidi wa kuhudumia wageni katika semina inayoendelea jijini Arusha katika Ukumbi wa AIM Mall.

Dkt. Abbasi ametoa mada kuhusiana na Majukumu ya Waongoza Watalii katika Kulinda Chapa (Branding) ya Nchi iliyobeba anuani ya: “ National/ Destination Branding and the Role of Tour Guides.” 

Katibu Mkuu huyo ambaye pia ni mtaalam wa masuala ya mawasiliano kwa umma, ametoa mfano wa mafanikio ya filamu ya “Tanzania: The Royal Tour” kuwa moja ya ushuhuda wa umuhimu wa nchi kuwekeza katika mikakati mikubwa ya kuiweka chapa yake katika ramani ya dunia.

“Sote hapa tutakiri kuwa Royal Tour ilifanikiwa sana na inabaki kuwa moja ya miradi yetu mikubwa kama Taifa ya kuitangaza Tanzania uliolipa sana. Nawahakikishieni tunakuja na mipango zaidi ya kuipeleka chapa ya Tanzania kimataifa zaidi,” alisema.

Amewapa mifano mbalimbali waongoza watalii hao jinsi nchi nyingi duniani zinavyowekeza katika kusambaza  habari nzuri na vivutio vyao vya utalii zaidi badala ya kulalamika au kuainisha changamoto zaidi.

“Kuna nadharia (theory) katika mawasiliano kwa umma inasema mtu akilitangaza jambo sana na kulirudiarudia (agenda setting) hata kama ni la uongo litaanza kuaminika. 

Sisi ni mabalozi wa utalii basi tukayaoneshe na kuyasema mazuri ya vivutio vyetu badala ya kuposti vitu vidogo vidogo vyenye changamoto,” alisema akionesha mifano ya baadhi ya nchi zinavyotumia nguvu kubwa kutangaza vivutio vyao japo ni vichache na haviizidi Tanzania. 

Mafunzo hayo yameandaliwa na Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kushirikiana na Chama cha Wamiliki wa Kampuni za  Utalii Tanzania(TATO) na yanafanyika kwa awamu (batches) kadhaa zenye washiriki zaidi ya 250 kila moja na lengo ni kuwafikia waongoza watalii zaidi ya 2,500 ikiwa ni maandalizi ya msimu mpya wa utalii lakini na matukio makubwa kama Afcon 2027.

Kwa mujibu wa takwimu za Benki Kuu ya Tanzania, watalii wa kimataifa nchini wameongezeka kutoka 922,000 mwaka 2021 kabla ya Royal Tour na kufikia 2,294,000 mwaka jana huku mapato ya jumla ya sekta ya utalii yakifikia Dola Bilioni 4.4 kutoka Bilioni 1.3 mwaka 2021 kabla ya Royal Tour.








Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2026, Ndugu Wazo Mwang’onda, ameipongeza TARURA wilaya ya Ruangwa kwa usimamizi mzuri wa mradi wa barabara ya Mwilala yenye urefu wa kilomita 0.59 kwa kiwango cha lami.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa barabara hiyo, Mwang’onda alisema ameridhishwa na ubora wa ujenzi huo ambao umejumuisha mitaro na kusimamiwa kwa viwango bora. 

Meneja wa TARURA wilaya ya Ruangwa, Mhandisi Mashaka Nalupi alisema mradi huo uliojengwa na M/S JATL TECH & CONSTRUCTION COMPANY LIMITED umegharimu shilingi 513,320,500.00.

Lengo la mradi ni kuboresha usafirishaji kwa wakazi wa vijiji vya Likangara, Dodoma, Nachingwea na Mchanganindani. Mhandisi Nalupi aliongeza kuwa barabara ya lami imepunguza kwa kiasi kikubwa gharama za ukarabati wa mara kwa mara.

Wananchi wa Ruangwa wamesema barabara hiyo imeleta faraja, kwani sasa wanaweza kufanya biashara hata nyakati za usiku kutokana na kuwepo kwa taa za barabarani. 








WWakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA) umechukua hatua madhubuti ya kuhamasisha matumizi ya nishati safi kwa kuwagawia watumishi wake majiko ya umeme, ikiwa ni sehemu ya juhudi za makusudi za kuhamasisha mabadiliko ya matumizi ya nishati nchini.

Akizungumza katika tukio hilo, Mkurugenzi wa Uendeshaji wa PBPA, Mhandisi Bruno Tarimo, amesema hatua hiyo inalenga kuimarisha juhudi za taasisi katika kuelimisha jamii kuhusu matumizi ya nishati safi na salama kwa matumizi ya kila siku.

Ameeleza kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia sera mbalimbali za kitaifa na kimataifa, imeendelea kutambua umuhimu wa nishati safi ya kupikia kama nyenzo muhimu ya kukabiliana na changamoto za kimazingira, kiafya, kijamii na kiuchumi.

“PBPA inatekeleza jukumu muhimu katika kusaidia juhudi za Serikali za kuhakikisha asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034. Ugawaji wa majiko janja aina ya pressure cooker kwa watumishi ni sehemu ya mkakati huo,” amesema Tarimo.

Aidha, amewataka wanufaika wa majiko hayo kuyatumia ipasavyo na kuwa mabalozi wa kuhamasisha matumizi ya nishati safi katika jamii zao ili kuongeza uelewa na kuharakisha mabadiliko ya matumizi ya nishati nchini.

Kwa upande wake, Afisa Dawati wa Nishati Safi ya Kupikia kutoka PBPA, Bi. Hilda Kowero, amesema kuwa Serikali imeweka mkakati maalum wa nishati safi ya kupikia unaolenga kuboresha maisha ya wananchi kupitia matumizi ya teknolojia rafiki kwa mazingira.

Amefafanua kuwa matumizi ya majiko ya umeme husaidia kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa, hivyo kulinda misitu, kupunguza ukataji wa miti na kuboresha afya kwa kupunguza madhara ya moshi yanayosababisha magonjwa ya njia ya hewa.

Katika kuhakikisha matumizi sahihi na salama ya majiko hayo, watumishi walipatiwa mafunzo maalum kuhusu namna bora ya kuyatumia, kutunza na kuzingatia tahadhari za usalama. Mafunzo hayo yalijumuisha matumizi sahihi ya umeme, njia za kupunguza matumizi ya nishati, pamoja na mbinu za kupika kwa ufanisi kwa kutumia majiko ya shinikizo (pressure cooker). Hatua hiyo inalenga kuwajengea watumishi uelewa wa kina ili waweze kunufaika kikamilifu na teknolojia hiyo na kueneza maarifa hayo kwa jamii inayowazunguka.

Bi. Kowero ameongeza kuwa PBPA itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhamasisha mabadiliko ya tabia kwa wananchi ili kuongeza matumizi ya nishati safi na kuchangia katika ujenzi wa jamii yenye afya bora na mazingira endelevu. 






Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.), ameagana na Balozi mteule wa Tanzania katika Jamhuri ya Korea Mhe. Balozi Noel E. Kaganda. 

Akizungumza katika kikao hicho kilichofanyika tarehe 30 Aprili, 2026 katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam, Waziri Kombo amemsii Balozi Kaganda kuendeleza ushirikiano wa kimkakati uliopo baina ya Tanzania na Jamhuri ya Korea, hususan katika sekta za uchumi wa buluu, elimu, miundombinu, teknolojia, viwanda, biashara, uwekezaji, afya na utalii. 

Aidha, amemsisitiza kufuatilia utekelezaji wa makubaliano yote yaliyofikiwa baina ya nchi hizi mbili, ikiwemo utekelezaji wa miradi iliyosainiwa wakati wa ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, mwezi Juni 2024.

Kwa upande wake, Balozi Kaganda amemshukuru Waziri Kombo kwa nasaha na miongozo yake na kuahidi kutekeleza diplomasia ya uchumi kwa vitendo kwa maslahi ya taifa. 

Kikao hicho pia kilihudhuriwa na Katibu Mkuu wa Wizara, Balozi Dkt. Samwel W. Shelukindo, ambaye aliungana na Waziri Kombo kumtakia Balozi Kaganda uwakilishi mwema huko Seoul, Jamhuri ya Korea.






Top News