Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma 

Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeendelea kuandika historia katika sekta ya miundombinu baada ya kufanikisha ujenzi wa zaidi ya kilometa 1,495 za barabara kwa kiwango cha lami pamoja na madaraja makubwa 18 ndani ya kipindi cha miaka mitano.

Mafanikio hayo yametajwa kuwa sehemu ya mageuzi makubwa yanayoendelea kufanyika nchini katika kuimarisha sekta ya uchukuzi na usafirishaji, hatua inayolenga kurahisisha huduma za kijamii, kukuza biashara na kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Akizungumza bungeni jijini Dodoma leo Jumatano Mei 20, 2026 wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Ujenzi kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, amesema Serikali imepiga hatua kubwa katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya barabara na madaraja katika maeneo mbalimbali nchini.

Amesema katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya Sita, jumla ya kilometa 1,495.45 za barabara zimejengwa kwa kiwango cha lami huku madaraja makubwa 18 yakijengwa au kuendelea kujengwa, jambo ambalo limeongeza ufanisi wa usafiri na kuchochea shughuli za kiuchumi mijini na vijijini.

Kwa mujibu wa Waziri Ulega, mtandao wa barabara za kitaifa unaosimamiwa na TANROADS umefikia kilometa 37,734.41, ambapo kati ya hizo kilometa 12,225.26 tayari zimejengwa kwa kiwango cha lami.

Ameeleza kuwa mafanikio hayo yanaonesha namna Serikali ilivyoongeza kasi ya uwekezaji katika sekta ya miundombinu ikilinganishwa na miaka ya nyuma, akibainisha kuwa wakati Tanzania inapata uhuru mwaka 1961, nchi ilikuwa na kilometa 1,360 pekee za barabara za lami.


Aidha, amesema kuanzia Serikali za Awamu ya Kwanza hadi Awamu ya Tano, jumla ya kilometa 9,369.81 za barabara za lami zilikuwa zimejengwa, huku Serikali ya Awamu ya Sita ikiendelea kuongeza kasi kubwa ya utekelezaji wa miradi hiyo kwa muda mfupi.

“Serikali imeendelea kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika sekta ya miundombinu kwa lengo la kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za usafiri na usafirishaji pamoja na kufungua fursa za kiuchumi katika maeneo mbalimbali ya nchi,” amesema Waziri Ulega.

Katika utekelezaji wa bajeti ya mwaka wa fedha 2025/2026, Waziri huyo amesema Wizara ya Ujenzi ilipanga kujenga na kukarabati barabara kuu na za mikoa zenye urefu wa kilometa 450 kwa kiwango cha lami pamoja na kilometa 820 kwa kiwango cha changarawe.

Hata hivyo, hadi kufikia Aprili 2026, Serikali ilikuwa imefanikiwa kukamilisha ujenzi na ukarabati wa kilometa 243.13 za barabara kwa kiwango cha lami pamoja na kilometa 94.36 kwa kiwango cha changarawe.


Kwa upande wa madaraja, Waziri Ulega amesema Serikali imekamilisha ujenzi wa madaraja tisa ambayo ni Mitomoni mkoani Ruvuma, Mirumba mkoani Katavi, Nzali mkoani Dodoma, Doma, Chakwale na Nguyami mkoani Morogoro, Mkili mkoani Ruvuma, Kalebe mkoani Kagera pamoja na Itembe mkoani Simiyu.


Amesema ujenzi wa madaraja mengine 11 unaendelea katika maeneo mbalimbali nchini, huku Serikali ikiendelea na maandalizi ya utekelezaji wa miradi mipya ya madaraja 13.


Mbali na hilo, Serikali pia inaendelea na kazi za upembuzi yakinifu pamoja na usanifu wa kina kwa baadhi ya miradi ya madaraja yenye lengo la kuboresha miundombinu ya usafiri katika maeneo yenye changamoto za mawasiliano wakati wa mvua na mafuriko.


Waziri Ulega amesema maboresho hayo ya miundombinu yanaendelea kuwa chachu ya ukuaji wa sekta mbalimbali ikiwemo biashara, kilimo, utalii na uwekezaji, huku wananchi wakinufaika na kupungua kwa muda wa safari pamoja na gharama za usafirishaji wa bidhaa na huduma.

Amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kusimamia utekelezaji wa miradi ya kimkakati kwa kuhakikisha barabara na madaraja yanajengwa kwa viwango vinavyokidhi mahitaji ya sasa na ya baadaye ya Watanzania.

“Dhamira ya Serikali ni kuhakikisha mtandao wa barabara unaendelea kuimarika ili kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini,” amesema Waziri Ulega.



 

Na Belinda Joseph -Dodoma.

Hafla ya kuhitimisha mafunzo ya mradi wa Rise Mamalishe imefanyika jijini Dodoma baada ya kuwafikia zaidi ya Mamalishe 3,000 kutoka mikoa mitano nchini, kupitia mradi uliotekelezwa kwa kipindi cha miaka mitatu ukiratibiwa na Stanbic Bank.

Akizungumza Mei 19 Jijini Dodoma, katika hafla hiyo, Meneja wa Stanbic Bank tawi la Dodoma, Joan Mbise, amesema mradi huo umewawezesha Mamalishe kuendelea kufanya biashara zao kwa ufanisi huku wakiboresha maisha yao na kukuza uchumi wao.

Amesema kati ya Mamalishe hao, zaidi ya 2,000 wamefikiwa kupitia mikopo ya mzunguko, huku Mamalishe 200 tayari wakisajiliwa na SIDO, kupata vyeti pamoja na vitambulisho vinavyowatambua rasmi kama wajasiriamali.

“Lengo letu ni kuhakikisha ujuzi wao unaimarika, biashara zao zinakua na jamii inanufaika. Kupitia mafunzo haya wameweza kuongeza thamani ya biashara zao na kuendesha shughuli zao kwa weledi zaidi,” amesema Mbise.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa mafunzo na usimamizi wa Mikoa, kutoka SIDO, CPA George Kasinga amesema programu ya Rise Mamalishe imekuwa chachu muhimu katika kuwawezesha wanawake wajasiriamali na kukuza biashara ndogondogo nchini.

Amesema SIDO imeendelea kutoa mafunzo na ushauri kwa wafanyabiashara ili kuhakikisha wanapata ujuzi wa kuendeleza biashara zao pamoja na kuongeza ushindani sokoni.

Aidha, washiriki wa programu hiyo wamekuwa wakipatiwa elimu ya fedha, usalama wa chakula, mbinu za kuongeza thamani ya bidhaa na namna ya kuvutia wateja, hatua inayolenga kuongeza fursa za kiuchumi na kuwasaidia kupata mikopo pamoja na matumizi sahihi ya mitaji.

Baadhi ya Mamalishe waliohitimu mafunzo hayo wameipongeza Stanbic Bank kwa kuandaa programu hiyo wakisema imewaongezea maarifa na ujuzi uliowasaidia kuongeza kipato na kuboresha huduma kwa wateja wao.

Wameahidi kutumia elimu waliyoipata kuwasaidia pia wafanyabiashara wengine katika jamii zao ili kuongeza maendeleo ya kiuchumi.



 

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo ya Ushirika nchini (Coop-Bank), Godfrey Ng’urah, amesema benki hiyo imejipanga kuhakikisha wakulima wanalipwa asilimia 50 ya fedha zao kabla ya mnada kufanyika na asilimia 50 iliyobaki kulipwa baada ya mnada, hatua inayolenga kuongeza uwazi na kuharakisha malipo kwa wakulima.

Mura aliyasema hayo mbele ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Mwigulu Nchemba, wakati alipotembelea banda la benki hiyo katika kilele cha maadhimisho ya miaka 20 ya Bodi ya Mfumo wa Stakabadhi za Ghala yaliyofanyika Mei 19 jijini Dodoma. 

Alieleza kuwa mkakati huo utasaidia kuondoa changamoto ya ucheleweshaji wa malipo ambayo imekuwa ikiwakwamisha wakulima katika shughuli zao za uzalishaji.

Aidha, alisema Coop-Bank itaendelea kushirikiana kwa karibu na vyama vya ushirika na wadau wa sekta ya kilimo ili kuwawezesha wakulima kupata huduma za kifedha kwa wakati, jambo litakaloongeza tija katika uzalishaji na kuimarisha uchumi wa wakulima pamoja na maendeleo ya sekta ya kilimo.



Na. Vero Ignatus, ​ARUSHA

Serikali ipo katika mchakato wa kuharakisha uundaji wa Sera ya Taifa ya Matumizi ya Akili Unde (AI) ili kuweka mfumo rasmi utakaohakikisha teknolojia hiyo inatumika kwa maadili, usalama, na kwa manufaa ya wananchi katika sekta mbalimbali za uzalishaji na huduma nchini.

​Hayo yamebainishwa leo, Mei 19, 2026, jijini Arusha na Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Sayansi na Teknolojia kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dk. Haroun Makandi, wakati akizungumza kwenye Kongamano la Kitaifa la QR Code na Akili Unde (NAIC 2026).

​Dk. Makandi amesisitiza kuwa, wakati matumizi ya AI yakizidi kushika kasi, serikali inaweka msisitizo mkubwa kwenye suala la maadili wakati wa uundaji na utumiaji wa mifumo hiyo ili kwenda sambamba na mapinduzi ya kidijitali yanayoendelea duniani.

​Mapinduzi Kwenye Kilimo, Afya na Elimu

​Katika kongamano hilo, wadau wamebainisha kuwa teknolojia ya AI ina uwezo mkubwa wa kuwa mkombozi wa maendeleo kwa kurahisisha kazi, kuongeza uzalishaji, na kupunguza gharama kupitia sekta kuu tatu:

​Kilimo: Inasaidia wakulima kupata taarifa sahihi za utabiri wa hali ya hewa, utambuzi wa magonjwa ya mimea, na mifumo ya masoko.

Katika sekta ya ​Afya: Inatumika kama chombo muhimu cha kufanya uchunguzi wa magonjwa kwa haraka na usahihi wa hali ya juu, jambo linalookoa maisha na kupunguza msongamano hospitalini.

​Elimu: Inajenga mfumo wa "mwalimu msaidizi wa kidijitali" anayeweza kutoa mafunzo ya mtu mmoja mmoja kulingana na uwezo wa mwanafunzi.

​Kukuza Kiswahili na Huduma za Serikali

​Zaidi ya hayo, AI imeonekana kuwa na mchango mkubwa katika kuboresha, kukuza, na kuratibu lugha ya Kiswahili kidijitali. Hatua hii inatajwa kusaidia kukieneza Kiswahili kimataifa kupitia mifumo ya kisasa ya ufasiri na uchambuzi wa maandishi, ​Mbali na sekta hizo, teknolojia hii inatajwa kusaidia utoaji wa huduma serikalini kwa kuongeza uwazi na ufanisi wa kiutendaji.

​Naye Mkurugenzi wa Scan Code, Faustine Mgimba, akizungumzia kasi ya teknolojia hiyo, ameungana na wataalamu wengine kusisitiza umuhimu wa kuwa na sera na sheria thabiti zitakazolinda faragha za wananchi na usalama wa taarifa (data privacy).

​Kongamano la NAIC 2026 limekuwa jukwaa muhimu lililokutanisha wadau wa teknolojia, watunga sera, na wabunifu kuweka mikakati ya pamoja. Lengo kuu ni kuhakikisha Tanzania haiachwi nyuma katika Mapinduzi ya Nne ya Viwanda (4IR), huku ikilinda misingi ya kitamaduni na usalama wa nchi kupitia udhibiti thabiti wa mifumo hiyo ya kidijitali.



▪️Azindua Mkakati wa Uhamasishaji wa Matumizi ya Mfumo wa Stakabadhi za Ghala

▪️Ataka wakulima walipwe fedha za awali badala ya kukopwa mazao

▪️Aagiza matumizi ya lumbesa yakomeshwe katika biashara ya mazao

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema asilimia 20 ya mapato yatokanayo na mazao ya kilimo inapaswa kuelekezwa katika ujenzi wa maghala karibu na maeneo ya uzalishaji ili kupunguza gharama kwa wakulima na kuongeza ufanisi wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala nchini.

“Asilimia 20 ya mapato yanayotokana na mazao ya kilimo inapaswa kuelekezwa katika ujenzi wa maghala kwenye maeneo ya uzalishaji ili wakulima wasipate shida ya kusafirisha mazao yao umbali mrefu,” amesema.

Waziri Mkuu amesema hayo leo Mei 19, 2026 alipokuwa mgeni rasmi katika kilele cha maadhimisho ya miaka 20 ya Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) yaliyofanyika katika Ukumbi wa Jakaya Kikwete Convention Centre jijini Dodoma, yenye kaulimbiu isemayo “Mfumo Imara, Uchumi Endelevu.”

Katika hafla hiyo, Waziri Mkuu pia alizindua rasmi Mkakati wa Uhamasishaji wa Matumizi ya Mfumo wa Stakabadhi za Ghala unaolenga kuongeza uelewa na ushiriki wa wakulima, wafanyabiashara, vyama vya ushirika, taasisi za fedha pamoja na wadau wengine katika matumizi ya mfumo huo nchini.

Dkt. Mwigulu amesema Serikali itaendelea kuimarisha mfumo huo kwa kuwa umechangia kuongeza uwazi na ushindani katika biashara ya mazao pamoja na kuhakikisha wakulima wananufaika na thamani halisi ya mazao yao.

“Pale ambapo kuna changamoto, mbadala wake si uholela. Mbadala wake ni kushughulikia changamoto zinazojitokeza,” amesema.

Aidha, amesema changamoto ya umbali wa maghala haitatatuliwa kwa kurejesha mifumo isiyo rasmi ya biashara ya mazao bali kwa kujenga maghala karibu na maeneo ya uzalishaji.

“Jawabu la changamoto ya umbali wa maghala si kurejesha uholela. Jawabu ni kujenga maghala karibu na wananchi ili wakulima wasipate shida ya kusafirisha mazao yao umbali mrefu,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Serikali kwa kushirikiana na taasisi za fedha inaandaa utaratibu wa kuwawezesha wakulima kupata malipo ya awali kupitia mazao yaliyohifadhiwa ghalani ili kuwaondoa katika changamoto ya kukopwa mazao au kuuza kwa hasara.

Pia amesema Serikali inaendelea na maandalizi ya mabadiliko ya sheria yatakayoruhusu mali zinazohamishika kutumika kama dhamana ikiwemo stakabadhi za ghala.

“Tunataka stakabadhi ya ghala iwe dhamana inayoweza kumwezesha mkulima kupata fedha wakati akisubiri bei nzuri ya mazao yake,” amesema.

Kadhalika, Waziri Mkuu amesisitiza matumizi ya vipimo rasmi na vifungashio vinavyokidhi viwango huku akieleza kuwa matumizi ya “lumbesa” hayapaswi kuendelea katika biashara ya kisasa ya mazao.

“Lumbesa ni jambo la zamani. Ni namna ya kumwibia mzalishaji mbele ya macho yake. Tuachane nalo,” amesema.

Aidha, amezitaka taasisi za fedha kurahisisha upatikanaji wa mikopo midogo kwa wakulima, wafugaji na wafanyabiashara wadogo ili waweze kutumia huduma rasmi za kifedha badala ya kukimbilia mikopo isiyo rasmi yenye madhara.

Waziri Mkuu amesema Serikali itaitisha kikao cha kitaifa kwa njia ya mtandao kitakachoshirikisha mikoa na wilaya zote kwa lengo la kufanya tathmini ya utekelezaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala na kupokea mapendekezo ya namna bora ya kuondoa changamoto zinazojitokeza katika maeneo mbalimbali.

Awali, Waziri wa Viwanda na Biashara, Bi. Judith Kapinga amesema mafanikio ya miaka 20 ya Mfumo wa Stakabadhi za Ghala yametokana na uwekezaji na usimamizi madhubuti unaoendelea kufanywa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya WRRB, Bi. Geraldine Rasheli amesema mfumo huo umeendelea kuwa nyenzo muhimu ya kuimarisha biashara ya mazao, kuongeza uwazi wa masoko na kuwawezesha wakulima kupata bei zenye tija.

Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo, Mhe. Deodatus Mwanyika amesema Bunge litaendelea kushirikiana na Serikali kuhakikisha mfumo huo unakuwa chachu ya maendeleo ya sekta za uzalishaji nchini.











Na Farida Mangube

Kamishna wa Kamisheni ya Polisi Jamii, Alex Mkama, amesema mmomonyoko wa maadili katika jamii umeendelea kuwa moja ya vyanzo vinavyochochea uhalifu, rushwa na kuporomoka kwa imani ya wananchi kwa taasisi za umma.

Mkama amesema hayo katika Chuo cha Maafisa wa Polisi Kidatu (TPSC Kidatu), wilayani Kilombero mkoani Morogoro, wakati akifunga Mafunzo ya Uongozi Mdogo Ngazi ya Sajini Awamu ya Pili ya mwaka wa mafunzo 2025/2026, ambapo askari 774 wamehitimu.

Amesema ili kulinda amani ya nchi, askari wa polisi wanapaswa kuwa waadilifu, waaminifu na wenye uwezo wa kusikiliza wananchi pamoja na kuwapatia mrejesho kuhusu hatua zinazochukuliwa katika mashauri yao.

Pia amewataka viongozi wa dini kuendelea kutumia majukwaa yao kuelimisha jamii juu ya umuhimu wa maadili na ushiriki wa wananchi katika ulinzi na usalama wa nchi.

Mkama ameonya kuwa matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii yanaweza kuwa chanzo cha taharuki na kuhatarisha usalama wa taifa iwapo hayatadhibitiwa na kuwataka askari wasijiingize katika matumizi hayo mabaya.

Mkuu wa Chuo hicho, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi Zarau Mpangule, amesema mafunzo yaliyotolewa yamejikita katika mambo mbalimbali ikiwemo sheria, uchunguzi wa makosa ya jinai, haki za binadamu, polisi jamii, usalama barabarani, kupambana na ugaidi pamoja na mbinu za medani na kivita.

Amesema chuo kinaendelea kuimarisha uwezo wa wakufunzi wake, ambapo 17 wanaendelea na mafunzo ya kujiendeleza kitaaluma ndani na nje ya nchi, ikiwemo Urusi, Korea Kusini, Uturuki na Singapore.

SACP Mpangule amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na uongozi wa Jeshi la Polisi kwa kuendelea kuwekeza katika mafunzo ya askari, huku akiwataka wahitimu kutumia maarifa waliyoyapata kuongeza ufanisi katika kazi ya polisi na kuchangia maendeleo ya taifa.







Kampuni ya Climb Up Limited imeeleza kuwa matumizi ya mizani janja ya kidigitali yanaweza kuwa suluhisho muhimu katika kuondoa changamoto za udanganyifu wa vipimo zinazowakabili wakulima, wafugaji na wafanyabiashara nchini.

Akizungumza jijini Dodoma wakati wa maadhimisho ya miaka 20 ya Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala, Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo, Emmanuel Ngallah, amesema teknolojia hiyo imeundwa kwa mfumo wenye ulinzi wa hali ya juu unaosaidia kuhakikisha vipimo haviwezi kuchezewa wala kufanyiwa udanganyifu.

Katika maadhimisho hayo, Waziri Mkuu wa Tanzania, Mwigulu Nchemba, alitembelea banda la Climb Up Limited kwa kushirikiana na WMA na kupata fursa ya kujionea namna mizani hiyo ya kidigitali inavyofanya kazi pamoja na mchango wake katika kuongeza uwazi na usahihi wa vipimo kwenye shughuli za biashara na kilimo.

Ngallah amesema kuwa  kampuni hiyo kwa kushirikiana na Wakala wa Vipimo imeendelea kuleta maboresho ya kidigitali yatakayosaidia kuongeza ufanisi na kuimarisha imani kwa watumiaji wa mifumo ya vipimo nchini.

Aidha, kampuni hiyo imebainisha kuwa matumizi ya mifumo ya kidigitali kupitia stakabadhi za ghala yamerahisisha uhifadhi wa taarifa za wakulima na usimamizi wa mazao yanayohifadhiwa maghalani, jambo linalochangia kuongeza ufanisi katika sekta ya kilimo na biashara.







Na Karama Kenyunko Michuzi Tv
JAMII imetakiwa kuguswa na kushiriki katika malezi ya watoto yatima pamoja na wale wenye mahitaji maalum wanaoishi katika vituo mbalimbali vya kulelea watoto, ili kuwapatia mazingira bora ya makuzi na maisha yenye matumaini.

Wito huo umetolewa na Umoja wa Wastaafu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) wakati walipotembelea Makao ya Watoto Wetu Tanzania yaliyopo Mbezi pamoja na Kituo cha Watoto wenye Usonji cha Norca Upendo kilichopo Kimara jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya utaratibu wao wa kila mwaka wa kutoa misaada ya kijamii.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo ya upendo, mmoja wa wastaafu hao, George Israel, alisema jamii inapaswa kuacha tabia ya kuwaficha watoto wenye changamoto za usonji majumbani, badala yake iwapeleke katika vituo maalum vinavyoweza kuwasaidia kupata matibabu na malezi sahihi.

Aidha, aliwataka wananchi kuwaunga mkono walezi wa vituo hivyo kwa kuwapatia mahitaji mbalimbali ili kuwatia moyo kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kuwalea watoto hao.

“Tumejionea mambo makubwa sana. Naiomba jamii iendelee kutoa misaada na kushirikiana na watu wenye maono haya ya kuwalea watoto wenye uhitaji,” alisema Israel.

Kwa upande wake, Mratibu wa ziara hiyo, Lukasi Kaigalula, alisema umoja huo umeendelea na utaratibu wa kujichanga kila mwaka kwa lengo la kuwasaidia watoto yatima na wale wanaolelewa katika mazingira magumu.

“Wastaafu tunajichanga na kuwaletea watoto hawa mahitaji mbalimbali. Kuna kila sababu ya kuwapa moyo wale wote waliojitolea kuwalea watoto hawa,” alisema Kaigalula.

Naye Catherine Mkelebe alitoa rai kwa jamii kupunguza migogoro ya kifamilia na ndoa, akisema hali hiyo imekuwa chanzo cha kuongezeka kwa watoto wanaokosa malezi ya wazazi au walezi.

“Migogoro ya ndoa si jambo zuri, kwani wanaoumia zaidi ni watoto. Tunawaasa wazazi watimize wajibu wao wa malezi ili kulinda ustawi wa watoto,” alisema.

Kwa upande wake, mlezi wa Kituo cha Norca Upendo, Grace Flavian Mauki, alisema kituo hicho kilianza kwa kulea watoto wawili pekee, lakini sasa kina watoto zaidi ya 50, hali inayoonyesha ukubwa wa changamoto hiyo katika jamii.

Alisisitiza kuwa watoto wenye usonji hawapaswi kufichwa majumbani, kwani wanaweza kusaidiwa kupitia mazoezi tiba na huduma maalum zinazotolewa katika vituo vya malezi.

“Tunaiomba jamii isiwafiche watoto hawa ndani. Wapelekwe kwenye vituo maalum kwa sababu wanaweza kusaidiwa na kupata maendeleo mazuri,” alisema.

Naye Mkurugenzi wa Makao ya Watoto Wetu Tanzania pamoja na Mwenyekiti wa Wamiliki wa Makao ya Watoto nchini, Evance Tegete, alisema kituo hicho kinajivunia kuwasaidia watoto waliotoka katika mazingira magumu hadi kufikia mafanikio makubwa ya kielimu na kijamii.

Alisema baadhi ya watoto waliowahi kulelewa katika makao hayo sasa ni wasomi na wananchi wenye mchango mkubwa katika jamii.

Wakihitimisha ziara yao, wastaafu hao walitoa wito kwa jamii kuendelea kuwalinda watoto, kuwathamini na kushiriki katika kuhakikisha wanapata malezi bora yatakayowawezesha kutimiza ndoto zao.





* Teknolojia ya ndani yafungua soko jipya la bidhaa za nyuki

* Sumu ya nyuki yatumika katika afya, vipodozi na tafiti za dawa

Na Karama Kenyunko

NYUKI ni miongoni mwa wadudu wenye umuhimu mkubwa duniani kutokana na mchango wao katika mazingira, afya ya binadamu na uchumi.

Tofauti na wadudu wengi wa kundi lao, nyuki huzalisha mazao mbalimbali yenye thamani kubwa kama asali, nta, propolis, chavua na sumu ya nyuki.

Ingawa asali na nta zimekuwa maarufu kwa muda mrefu, sumu ya nyuki bado haijafahamika kwa kiwango kikubwa kutokana na ukosefu wa elimu, teknolojia na uwekezaji katika uzalishaji wake.

Hata hivyo, kampuni ya Sensa Tanzania Limited imekuja na ubunifu mpya wa teknolojia ya kuvuna sumu ya nyuki, hatua inayotajwa kufungua ukurasa mpya kwa wafugaji wa nyuki nchini.

Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Patrick Kitosi, anasema amebuni na kutengeneza mashine maalumu za kuvuna sumu ya nyuki kwa kutumia teknolojia ya umeme na vifaa vya kielektroniki.

Anasema utafiti wa teknolojia hiyo ulianza mwaka 2021 ukiwa na lengo la kuwasaidia wafugaji wa nyuki kutumia fursa ya biashara ya sumu ya nyuki, ambayo ina thamani kubwa katika sekta ya afya na utengenezaji wa dawa.
Kitosi anasema mashine hizo hutumia mawimbi maalumu ya masafa yanayowavuta nyuki kusogea karibu na kifaa hicho.

"Nyuki wanapogusa sehemu ya mashine hupata msisimko mdogo wa umeme unaochochea utoaji wa sumu kama njia ya kujilinda," anasema.

Anaeleza kuwa sumu hiyo hukusanyika kwenye kifaa katika mfumo wa unga, ambapo mfugaji anaweza kuikusanya, kuipima kwa gramu na kuiuza katika masoko mbalimbali.

Kitosi anasema wafugaji wengi wamejikita zaidi kwenye uzalishaji wa asali na nta, huku bidhaa nyingine zinazotokana na nyuki zikiendelea kutofahamika kwa kiwango kikubwa.

"Mbali na asali, nyuki huzalisha pia chavua, gundi ya nyuki, maziwa ya nyuki na sumu ya nyuki, ambazo zote zina soko kubwa ndani na nje ya nchi," anafafanua.

Anaongeza kuwa sumu ya nyuki ina matumizi mbalimbali katika sekta ya afya ikiwemo kusaidia katika utengenezaji wa dawa na tafiti mbalimbali za kitabibu.

Katika sumu hiyo kuna kiambata kinachoitwa apitoxin ambacho tafiti mbalimbali zinaeleza kuwa na uwezo wa kusaidia katika matumizi ya kitabibu, ikiwemo kupunguza baadhi ya maumivu ya viungo na kusaidia tafiti zinazohusiana na matatizo ya mfumo wa neva.

Pia, baadhi ya viambata vilivyopo kwenye sumu hiyo vinaelezwa kuwa na uwezo wa kupambana na bakteria, fangasi na baadhi ya virusi.
Teknolojia Inavyofanya Kazi
Tofauti na njia za zamani ambazo zilikuwa ngumu na wakati mwingine kuathiri nyuki, mashine zilizobuniwa na Sensa Tanzania Limited zinaruhusu sumu kuvunwa bila kuwaua nyuki.

Kwa mujibu wa Kitosi, mzinga mmoja unaweza kutoa kati ya gramu 0.8 hadi 1.5 za sumu ndani ya takribani dakika 30, kutegemeana na idadi ya nyuki waliopo kwenye mzinga huo.

Mashine hizo hutengenezwa kulingana na mahitaji ya mfugaji, ambapo zipo zinazoweza kuvuna mzinga mmoja au mizinga mingi kwa wakati mmoja.

"Bei ya mashine ndogo inaanzia Sh 500,000 na huongezeka kulingana na uwezo wa kifaa. Changamoto kubwa iliyopo ni ukosefu wa elimu kuhusu biashara ya sumu ya nyuki pamoja na uhaba wa teknolojia za kisasa kwa wafugaji wengi nchini," anasema.
Fursa ya Soko la Kimataifa
Kwa mujibu wa Kitosi, masoko makubwa ya sumu ya nyuki yanapatikana katika nchi za India, China na Algeria ambako hutumika zaidi katika viwanda vya dawa.

Hata hivyo, amesema ubora wa sumu ya nyuki hutegemea mazingira pamoja na aina ya mimea ambayo nyuki wameitumia kupata chakula.

Anasema mwaka 2022 kampuni hiyo ilipata msaada wa Sh milioni 28 kutoka Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia kupitia mfuko wa sayansi na ubunifu, fedha zilizosaidia kuendeleza tafiti za teknolojia hiyo.

"Sensa Tanzania tunaamini teknolojia inaweza kusaidia kuongeza ajira kwa vijana na kuboresha sekta ya ufugaji wa nyuki nchini kupitia vifaa vinavyotengenezwa hapa Tanzania," anasema.

Ubunifu huo unaendana na Dira ya 2050 inayoweka mkazo katika kukuza uchumi shindani unaotumia maarifa, teknolojia na utafiti kuongeza uzalishaji na thamani ya bidhaa zinazotokana na rasilimali za asili.

Katika muktadha huo, bidhaa za nyuki kama sumu ya nyuki zinaweza kuwa sehemu ya uchumi mpya unaoendelea kukua duniani, huku sekta ya nyuki ikiendelea kuwa muhimu katika usalama wa chakula na uhifadhi wa mazingira.

Nyuki wanapoongeza shughuli za uchavushaji, huchangia kuongeza mavuno ya mazao ya kilimo pamoja na kuhifadhi bioanuwai na miti inayosaidia kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Kampuni hiyo yenye makao yake Magomeni, Dar es Salaam, inaendelea kufanya tafiti za teknolojia nyingine zitakazorahisisha uvunaji wa bidhaa mbalimbali zinazotokana na nyuki.

Naye Mshauri wa masuala ya uvunaji wa mazao ya nyuki, Yassin Masenga, anasema ufugaji wa nyuki una mchango mkubwa katika uhifadhi wa mazingira na uzalishaji wa chakula.

Kwa mujibu wake, nyuki husaidia uchavushaji wa mazao na mimea jambo linaloongeza mavuno kwa wakulima na kusaidia mazingira kuendelea kuwa salama kwa viumbe hai.

"Ufugaji wa nyuki si tu biashara ya asali, bali pia ni sehemu ya kulinda mazingira na kuongeza uzalishaji wa kilimo," anasema.

Masenga anasema sumu ya nyuki imekuwa ikitumika katika baadhi ya tiba za asili na maandalizi ya bidhaa mbalimbali zikiwemo za urembo na matumizi ya kitabibu.

Pia anaonya kuwa matumizi ya sumu hiyo yanahitaji tahadhari kwani hayapendekezwi kwa watu wenye matatizo makubwa ya mzio, upungufu wa damu au baadhi ya changamoto za kiafya.

Kwa upande wake, Ofisa Misitu Mkuu kutoka Wizara ya Mifugo, Dk Siima Bakengesa, anasema wanakaribisha bunifu zote zinazosaidia kuongeza thamani ya mnyororo mzima wa mazao ya nyuki kwa kuwa zinaweza kusaidia kuinua maisha ya wafugaji.

"Tunaamini kila ubunifu umepitia hatua mbalimbali kabla ya kuanza kutumika. Ndiyo maana tumekuja na Mpango Maalum wa Ufugaji kwa Tanzania iliyobora 2025 ili kuhakikisha bunifu zinazochangia maendeleo zinawafikia Watanzania hususan vijana na wanawake," anasema Dk Bakengesa.

Anasisitiza kuwa nyuki hutoa mazao mbalimbali ikiwemo asali, chavua, nta na sumu ya nyuki ambayo inaendelea kuvutia tafiti na matumizi mbalimbali.

Kadiri elimu, teknolojia na uwekezaji vinavyoendelea kuongezeka, sekta ya nyuki nchini inaweza kutoka kuwa chanzo cha asali pekee na kuwa kitovu kipya cha bidhaa zenye thamani kubwa katika uchumi wa Tanzania.

Na OWM - TAMISEMI, Dodoma

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amewasisitiza washiriki wa Mkutano wa Mwaka wa Tathmini ya Afua ya Uthibiti wa Taka Ngumu na Usafi wa Miji, kuhakikisha suala usafi wa mazingira linakuwa ajenda ya kudumu katika vikao vyote vitakavyofanyika katika ngazi zote za Mamlaka za Serikali za Mitaa ili kuwezesha miji na majiji nchini kuwa masafi.

Prof. Shemdoe ametoa maelekezo hayo Mei 12, 2026 jijini Dodoma wakati akifungua mkutano wa kwanza wa Mwaka wa Tathmini ya Afua ya Uthibiti wa Taka Ngumu na Usafi wa Miji, unaofanyika katika Ukumbi wa Hoteli ya Jiji- Mtumba, unaohudhuriwa na Maafisa Afya wa Mikoa, Maafisa Afya wa Halmashauri na Maafisa Mazingira wa Halmashauri.

“Nasisitiza suala la usafi wa mazingira liwe ajenda ya vikao vyenu. Vikao vya Kamati za Ushauri za Mikoa, Kamati za Ushauri za Wilaya, Kamati za Maendeleo za Kata, Mabaraza ya Madiwani, Kamati za Kudumu za Halmashauri pamoja na vya ALAT ngazi ya mkoa na taifa,” amesema Prof. Shemdoe.

Prof. Shemdoe ameainisha kuwa, usafi wa mazingira ukizingatiwa katika ngazi zote za Mamlaka ya Serikali za Mitaa utapunguza milipuko ya magonjwa na matumizi ya fedha kwa ajili ya ununuzi wa madawa, na fedha zitakazookolewa zitaelekezwa katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo, hivyo amewataka maafisa hao kufanya kazi kwa bidii na weledi ili kupunguza milipuko ya magonjwa na matumizi ya ununuzi wa dawa.

“Namshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuona umuhimu wa kuanzisha vitengo vya udhibiti wa taka ngumu ambavyo vinasaidia kuboresha zoezi la usafi wa mazingira nchini,” Prof. Shemdoe ameeleza.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa anayeshughulikia afya Prof. Tumaini Nagu amesema uthibiti wa taka kwenye halmashauri ni jambo muhimu katika kuhakikisha kunakuwa na usafi wa mazingira na udhibiti wa magonjwa ya milipuko na kuongeza kuwa, takwimu za kisayansi zinaeleza kwamba uthibiti madhubuti wa taka ngumu unapelekea kupungua kwa asilimia 30 hadi 40 za magonjwa kama Malaria na mengineyo ambayo yanadhibitiwa kwa usafi wa mazingira.

Akizungumza kwa niaba ya washiriki, Mkuu wa Kitengo cha Udhibiti taka ngumu wa Halmashauri ya wilaya Bahi Bw. William Mpangala amesema kuwa Serikali kupitia Mamlaka za Serikali za Mitaa inaendelea kushirikisha sekta binafsi katika utekelezaji wa afua za udhibiti wa taka ngumu kama za ukusanyaji na uchakataji wa taka ngumu, na kuongeza kuwa ushirikishwaji huo umeongeza ufanisi katika udhibiti wa taka kwenye halmashauri nchini.

Mkutano wa Mwaka huu una kaulimbiu isemayo “Taka ngumu ni Mali; tumia, rejeleza na Weka Miji katika hali ya usafi”.










Na Mwandishi Maalum
KATIKA zama hizi za utandawazi, mataifa mengi duniani yamekuwa yakitumia lugha zao kama silaha ya kujitangaza, kujenga ushawishi wa kiuchumi na kueneza utamaduni wao. Lugha zimekuwa zaidi ya mawasiliano. Sasa ni nyenzo muhimu za diplomasia, biashara, elimu na utambulisho wa taifa.

Kwa Tanzania, sasa ni zamu ya Kiswahili kung’ara kimataifa.
Hatua ya kufanyika kwa Kongamano la Kimataifa la Kiswahili jijini Paris, nchini Ufaransa kuanzia Julai 3 hadi 7, 2026 ni ishara kubwa kuwa lugha hiyo inaingia katika hatua mpya ya ukuaji na ushawishi duniani.

Kongamano hilo linaandaliwa na Serikali ya Tanzania kwa lengo la kuitangaza lugha ya Kiswahili pamoja na utamaduni wa Waswahili kwa mataifa mbalimbali duniani.
Kwa miaka mingi, Kiswahili kimekuwa uti wa mgongo wa umoja wa Watanzania na mataifa ya Afrika Mashariki. Sasa, kupitia juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan, lugha hiyo inaendelea kuvuka mipaka na kupata nafasi katika majukwaa makubwa ya kimataifa.

Paris kuwa Kitovu cha Kiswahili

Mkurugenzi wa Maendeleo ya Utamaduni nchini, Boniface Kadili amesema kongamano hilo lina lengo la kueneza lugha ya Kiswahili katika mataifa ambayo hayajawahi kuizungumza wala kuifahamu kwa undani.

Amesema kongamano hilo ni la pili kufanyika kimataifa baada ya lile la kwanza lililofanyika Oktoba mwaka 2022 jijini Havana, Cuba.

“Kongamano hili lina maana kubwa kwa sababu lugha ya Kiswahili na utamaduni wake vitawafikia watu wa mataifa mbalimbali duniani,” amesema Kadili.

Kwa mujibu wake, hatua hiyo inafuatia uamuzi wa UNESCO kuitambua Kiswahili mwaka 2021 kama lugha yenye hadhi ya kimataifa na kutenga Julai 7 kuwa Siku ya Kiswahili Duniani.

Kadili amesema serikali imejipanga kuhakikisha dunia inatambua kuwa Kiswahili si lugha ya mawasiliano ya kawaida tu. Ni lugha yenye uwezo wa kutumika katika siasa, uchumi, diplomasia, sayansi na teknolojia.

Kiswahili na Diplomasia ya Kimataifa
Wachambuzi wa masuala ya utamaduni wanaeleza kuwa mataifa yenye nguvu duniani yamefanikiwa kutokana na uwezo wao wa kueneza lugha zao.

China imewekeza katika kueneza Kichina kupitia taasisi za Confucius duniani kote. Wafaransa wanaendelea kulinda hadhi ya Kifaransa huku Waarabu wakitumia Kiarabu kama sehemu ya utambulisho na ushawishi wao wa kimataifa.

Kwa Tanzania, kupeleka Kiswahili katika mataifa mbalimbali ni hatua ya kimkakati inayoweza kuongeza ushawishi wa taifa katika diplomasia ya kimataifa.

Kadili anaeleza kuwa kongamano hilo halitakuwa tukio la kawaida la burudani. Ni sehemu ya harakati endelevu za kuifanya Kiswahili kuwa lugha yenye mashiko duniani.

“Kiswahili kinaendelea kuwa lugha yenye ushawishi mkubwa wa kimataifa. Tunataka iwe lugha ya kisiasa, uchumi na diplomasia za kimataifa,” amesema.

Utamaduni wa Mswahili Kutambulishwa

Mbali na lugha, kongamano hilo pia litatoa nafasi ya kuutambulisha utamaduni wa Waswahili kwa mataifa mengine.

Kwa mujibu wa Kadili, watu wengi duniani wamekuwa na ukakasi wa kujifunza Kiswahili kwa sababu hawajawahi kuujua utamaduni wa Waswahili.

Kupitia kongamano hilo, washiriki watapata nafasi ya kufahamu maisha ya Waswahili, mila, mavazi, vyakula, muziki, historia na sanaa mbalimbali za Afrika Mashariki.

Katika siku hizo za kongamano, Paris inatarajiwa kuwa jukwaa la maonesho ya sanaa za Kiswahili, filamu, muziki wa asili pamoja na vivutio vya utalii wa Tanzania.

Fursa za Kiuchumi Kupitia Kiswahili

Ukuaji wa Kiswahili kimataifa unaonekana pia kuwa fursa kubwa ya kiuchumi kwa Watanzania.

Kadili amesema watengeneza maudhui ya Kiswahili watanufaika zaidi kutokana na kutambuliwa kwa lugha hiyo na majukwaa makubwa ya kidijitali duniani kama TikTok, Meta na Google.
“Tunahitaji Watanzania watambue kwamba Kiswahili sasa kinatambulika kimataifa. Watu wanaotengeneza maudhui kwa Kiswahili wanapaswa kupata malipo sawa na watumiaji wa lugha nyingine za kimataifa,” amesema.

Hii ina maana kuwa vijana wanaojihusisha na video, filamu, muziki, vipindi vya mtandaoni na maudhui ya elimu kwa Kiswahili wanaweza kupata soko kubwa zaidi duniani.

Aidha, ukuaji wa Kiswahili utaongeza mahitaji ya wataalamu wa tafsiri na ukalimani. Wasomi wa lugha hiyo sasa wana nafasi kubwa zaidi ya ajira kutokana na kuongezeka kwa watu wanaohitaji kujifunza Kiswahili.

Kiswahili na Utalii wa Tanzania
Kupitia kongamano hilo, Tanzania pia itanufaika katika sekta ya utalii.
Kadili amesema sambamba na kongamano hilo, filamu mbalimbali za kuitangaza Tanzania zitaoneshwa ili kuhamasisha mataifa mengine kutembelea vivutio vya utalii vya nchi hiyo.

Katika miaka ya karibuni, Tanzania imeendelea kutumia diplomasia ya utalii kupitia miradi kama The Royal Tour, ambayo iliitangaza Tanzania duniani kupitia vivutio vyake vya asili, utamaduni na historia.

Dkt. Mnata Raysani, Mkurugenzi Msaidizi sehemu ya lugha katika Idara ya Utamaduni, anaeleza kuwa kuongezeka kwa watu wanaojifunza Kiswahili kunaweza kuongeza idadi ya watalii wanaotaka kuifahamu Afrika Mashariki na utamaduni wake.

Changamoto Zinazoikabili Kiswahili

Pamoja na mafanikio hayo, bado zipo changamoto zinazoikabili lugha ya Kiswahili, hasa kutoka kwa baadhi ya Watanzania wenyewe.

Raysani anasema baadhi ya wasomi bado wanaamini kuwa Kiswahili hakina hadhi ya kimataifa. Kutokana na hali hiyo, baadhi yao huwapa watoto wao kipaumbele zaidi lugha za kigeni kuliko Kiswahili.

“Baadhi ya watu wanaona Kiswahili si lugha ya kujifunza wala ya maendeleo. Hii ni changamoto kubwa ambayo tunapaswa kuikabili,” amesema.

Wataalamu wa elimu wanaonya kuwa dhana hiyo inaweza kudhoofisha juhudi za kukikuza Kiswahili ikiwa Watanzania wenyewe hawatakithamini.

Mhadhiri wa lugha kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Hamisi Mwansoko, anasema hakuna taifa lililoendelea kwa kuacha lugha yake.

“Lugha ni sehemu ya utu na maendeleo ya taifa. Mataifa makubwa duniani yameendelea kupitia lugha zao,” anasema.
Serikali Yaweka Msingi wa Kiswahili cha Kisasa
Serikali ya Tanzania inaamini kuwa njia bora ya kuondoa dhana potofu kuhusu Kiswahili ni kuonesha uwezo wake katika nyanja mbalimbali za kisasa.

Kadili amesema serikali imeamua kudhihirishia dunia kuwa Kiswahili kinaweza kutumika katika shughuli za sayansi, teknolojia, uchumi na diplomasia kama zilivyo lugha nyingine kubwa duniani.

Hatua hiyo inatajwa kuwa mwanzo wa safari mpya ambapo Kiswahili kinaweza kuwa moja ya lugha muhimu zaidi duniani katika miaka ijayo.

Hitimisho
Kongamano la Kimataifa la Kiswahili la mwaka 2026 si tukio la kawaida. Ni hatua muhimu ya Tanzania kujitambulisha upya duniani kupitia lugha na utamaduni wake.

Kiswahili sasa kinavuka mipaka ya Afrika Mashariki na kuingia katika ramani ya lugha kubwa duniani. Kadri mataifa mengi yanavyoanza kujifunza na kutumia Kiswahili, ndivyo nafasi ya Tanzania katika diplomasia, utamaduni, utalii na uchumi inavyozidi kuimarika.

Huu ni wakati wa Watanzania kujivunia lugha yao, kuitunza na kuitumia kama nyenzo ya maendeleo. Dunia inaanza kuisikia sauti ya Kiswahili, na safari yake ya kuwa lugha ya kimataifa sasa imeanza kwa kasi mpya.

Top News