MWENYEKITI wa Bodi ya Wakurugenzi wa Taasisi ya Tanzania Women Empowement Network (TAWEN) Balozi Amina Salum Ali, amesema viongozi na watumishi wanao wajibu kuhakikisha taasisi zao zinakuwa mfano wa kuigwa kutekeleza maelekezo ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan na sera ya kitaifa ya nishati safi.

Ameyasema hayo leo katika semina maalumu ya matumizi ya nishati safi, iliyoandaliwa na TAWEN na kushirikisha wakuu wa shule za sekondari za Wilaya ya Ubungo na wadau wa nishati na taasisi za kifedha.

Balozi Amina, amesema watumishi wanapaswa kuwa mabalozi wa mabadiliko hayo ya kuachana na nishati chafu na kuhamasisha familia na jamii zinazo wazunguka kutumia nishati safi.

Amesema dhamira ya Rais Dk. Samia, ambaye ni kinara wa matumizi ya nishati safi ya kupikia ni kuona jamii nzima ya watanzania inatumia nishati hiyo ambapo taasisi za elimu haziwezi kuachwa nyuma.

"Hivyo basi nyie wakuu wa shule ni watu muhimu katika kusaidia jitihada hizo za Rais Dk. Samia, kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa kutumianishati safi. Tunataka kila mtu katika jamii atumie fursa hii. Tumsaidie rais kuibeba ejenda hii muhimu,"ameeleza Balozi Amina.

Ameeleza, Rais Dk. Samia, ametoa maelekezo kwa taasisi zikiwamo shule za bweni kutumia nishati safi hivyo kupongeza TAWEN kutoa elimu hiyo kwa wakuu wa shule ambao ni wadau muhimu wa utekelezaji wa ajenda hiyo.

"Vilevile ninaipongeza TAWEN kwa kazi kubwa ya kuunganisha wadaiu, kuendesha makongamano ya kitaifa na kimataifa na kuhamasisha uwekezaji katika nishati safi. Hii ni ishara ya uongozi thabiti na dhamira ya kweli kuleta mabadiliko chanya kwa taifa letu,"ameeleza.

Awali Mkurugenzi Mtendaji wa Tawen, Florence Masunga, amesema lengo la semina hiyo ni kuhamasisha wakuu wa shule kutumia nishati safi shuleni, kuwapa fursa zinazo patikana kupitia uwekezaji katika nishati safi na fursa za kifedha hususan uwekezaji.

"Pia semina hii ili lenga kuwapa elimu wakuu wa shule ambayo itawafanya kuwa mabalozi wazuri wa matumizi ya nishati safi na kusaidia serikali chini ya Rais Dk. Samia, kufikia malengo ya watu wote katika jamii yetu kutumia nishati hii,"amesema Masunga.

Ameeleza, sekta ya nishati safi ina firsa nyingi ambapo wakuu wa shule wanaweza kuwekeza na kujiingizia kipato kitakacho wasaidia hata baada ya kustaafu.

Ameeleza TAWEN itaendelea kutoa elimu hiyo kwa jamii nzima ya kitanzania na hata nje ya nchi kwa kuibeba ajenda hiyo muhimu iliyoasisiwa na Rais Dk. Samia, ambayo inasaidia pia kulinda mazingira, kudumisha afya na ustawi wa jamii salama.

Ofisa Elimu ya Sekondari wa Wilaya ya Ubungo, Benedict Sandy, amewahimiza wakuu wa shule kuanza kutekeleza maelekezo ya serikali ya kutumia nishati safi na kwamba semina hiyo iwe chachu kwao.

"Tunawashukuru TAWEN kwa semina hii. Sasa iwe chachu kwetu kuanza utekelezaji wa maagizo ya serikali na kuibeba ajenda ya Rais Dk. Samia. Tuwe mabalozi, tuipeleke elimu hii kwa wanafunzi nao waipeleke katika jamii,"alisema Sandy.

Miongoni mwa taasisi zilizoshiriki semina hiyo ni Shirika la Madini Tanzania (STAMICO), Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Benki ya NMB, UTT Amis, Taifa Gas na PSSSF.








-Serikali yaja na mkakati wa kuongeza uzalishaji, kutoa mizinga 11,000

Sekta ya ufugaji nyuki nchini imepata msukumo mpya baada ya Serikali kutangaza mpango wa kutoa mizinga 11,000 pamoja na mafunzo kwa zaidi ya wafugaji 3,000 katika mwaka wa fedha 2026/2027, hatua inayolenga kuongeza uzalishaji wa asali na kuinua uchumi wa wananchi wanaotegemea shughuli hiyo.

Hatua hiyo ilibainishwa katika mdahalo mkubwa wa wadau wa sekta ya nyuki uliofanyika mkoani Tabora, ukihusisha wafugaji wa nyuki, wataalamu wa misitu na nyuki, taasisi mbalimbali pamoja na wadau wa maendeleo kujadili mikakati ya kuimarisha ufugaji wa kisasa na kuongeza thamani ya mazao ya nyuki nchini.

Akizungumza katika mdahalo huo, Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Tabora, Bi. Upendo Joseph Haule, aliyemwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, alisema ufugaji wa nyuki umeendelea kuwa chanzo muhimu cha ajira na kipato kwa wananchi wengi, hasa wanaoishi jirani na maeneo ya misitu.

Alisema Serikali inaendelea kuhimiza matumizi ya teknolojia bora, mizinga ya kisasa na uwekezaji katika uchakataji wa mazao ya nyuki ili kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika soko la kimataifa.

“ Mkoa umeendelea kuhamasisha uwekezaji katika uchakataji wa mazao ya nyuki, matumizi ya teknolojia bora pamoja na kuongeza thamani ya bidhaa za nyuki. Pia umeanzishwa wazo la kuunda Kongani la Ushindani wa Asali ya Tabora (Tabora Honey Competitive Cluster),” alisema Bi. Haule.

Alisema lengo la kongamano hilo ni kuwakutanisha wadau wote wa mnyororo wa thamani wa mazao ya nyuki ili kuongeza ubora na ushindani wa asali ya Tabora katika masoko ya ndani na nje ya nchi.

Bi. Haule alionya kuhusu ongezeko la matukio ya moto wa misitu yanayohatarisha shughuli za ufugaji nyuki katika baadhi ya maeneo na kusisitiza umuhimu wa jamii kushiriki kikamilifu katika uhifadhi wa mazingira na vyanzo vya chakula vya nyuki.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Misitu na Nyuki Wizara ya Maliasili na Utalii Bw, Daniel Pancrasi, alisema katika mwaka wa fedha 2025/2026 Serikali imetoa jumla ya mizinga 9,215 na kuwafikia wafugaji 4,934 kupitia mafunzo mbalimbali ya ufugaji wa kisasa wa nyuki.

Alisema katika mwaka ujao wa fedha, Serikali inalenga kuongeza utoaji wa mizinga hadi 11,000 sambamba na kuendelea kuwajengea uwezo wananchi ili sekta hiyo iwe chanzo kikubwa cha mapato ya kaya na taifa.

“Tunawaomba wananchi kuchangamkia fursa hii kwa kuingia kwenye ufugaji wa kisasa wa nyuki ambao una tija kubwa kiuchumi na kimazingira,” alisema Bw. Pancras.

Katika mdahalo huo, wadau walisisitiza umuhimu wa kuongeza thamani ya mazao ya nyuki kupitia usindikaji wa kisasa, ufungashaji bora na kuzingatia viwango vya ubora vinavyokubalika kimataifa ili bidhaa za Tanzania ziweze kushindana kwenye masoko ya nje.

Pia walipendekeza kuongezwa kwa mafunzo kwa vikundi vya wafugaji wa nyuki, hususan vijana na wanawake, ili waweze kushiriki kikamilifu katika uzalishaji, usindikaji na biashara ya mazao ya nyuki.

Wadau hao walieleza kuwa sekta ya nyuki ina uwezo mkubwa wa kuzalisha ajira, kuongeza mapato ya wananchi na kuchangia uhifadhi wa misitu, endapo uwekezaji wa kimkakati utaongezwa na ushirikiano kati ya Serikali, sekta binafsi na jamii utaimarishwa.







▪️Asisitiza ushirikiano wa kikanda katika kulinda rasilimali za ziwa
▪️Aagiza kuimarishwa kwa mifumo ya uokoaji na usalama majini
▪️Ataka matumizi ya teknolojia katika usimamizi wa rasilimali za maji


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki zinapaswa kuendelea kushirikiana kulinda na kulihifadhi Ziwa Victoria kwa kuwa ni rasilimali muhimu inayogusa maisha, uchumi na mustakabali wa mamilioni ya wananchi wa ukanda huo.

“Ziwa Victoria si mali ya nchi moja pekee. Ni rasilimali inayotuunganisha kama Jumuiya na tunapaswa kushirikiana katika kulinda mazingira, usalama na uchumi unaotegemea ziwa hili,” amesema Dkt. Nchemba.

Amesema hayo leo Alhamisi, Mei 21, 2026 wakati akizindua rasmi Siku ya Ziwa Victoria na kufunga kilele cha maadhimisho ya kwanza yaliyofanyika katika Viwanja vya Nanenane Nyamhongolo jijini Mwanza.

Kauli mbiu ya maadhimisho hayo ilikuwa “Maji Yetu, Mustakabali Wetu: Tuungane kwa Uendelevu wa Bonde la Ziwa Victoria.”

Katika hotuba yake, Waziri Mkuu amesema maadhimisho hayo yanapaswa kuwa sehemu ya kuhamasisha usimamizi endelevu wa rasilimali za maji, kuimarisha mshikamano wa kikanda na kuongeza uwajibikaji wa pamoja katika kulinda mazingira ya Ziwa Victoria.

Aidha, amesema Serikali itaendelea kushirikiana na nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki katika kuimarisha mifumo ya usalama majini, kudhibiti uharibifu wa mazingira na kuendeleza matumizi ya teknolojia katika usimamizi wa rasilimali za ziwa hilo.

“Sote tunawajibika kutunza mazingira ya Ziwa Victoria kwa manufaa ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesisitiza umuhimu wa kuimarishwa kwa mifumo ya uokoaji majini pamoja na matumizi ya mifumo ya kidijitali katika kufuatilia shughuli za uvuvi, ubora wa maji na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Pia ametoa wito kwa taasisi za utafiti kuendelea kufanya tafiti zitakazosaidia kupata suluhisho la changamoto mbalimbali zinazoathiri mazingira ya Ziwa Victoria ikiwemo ongezeko la magugu maji na uharibifu wa vyanzo vya maji.

Awali, Waziri wa Maji, Jumaa Aweso amesema Tanzania itaendelea kuwa mstari wa mbele katika kulinda na kuhifadhi Ziwa Victoria kwa kuwa ni nguzo muhimu ya uchumi, usalama na maendeleo ya wananchi wa ukanda wa ziwa.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, James Ole Millya amesema Tanzania itaendelea kushirikiana na nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki katika kuandaa na kutekeleza mipango ya pamoja ya kuhifadhi rasilimali za Bonde la Ziwa Victoria.

Naye Katibu Mtendaji wa Kamisheni ya Bonde la Ziwa Victoria, Masinde Bwire amesema maadhimisho hayo ni hatua muhimu ya kuimarisha dhamira ya pamoja ya nchi wanachama katika kulinda moja ya rasilimali kubwa za maji barani Afrika.

Wawakilishi kutoka Kenya na Uganda waliishukuru Tanzania kwa kuwa mwenyeji wa maadhimisho hayo na kusisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kikanda katika kukabiliana na changamoto za uchafuzi wa mazingira, mabadiliko ya tabianchi na usalama wa majini ndani ya Ziwa Victoria.

Katika maadhimisho hayo, Waziri Mkuu pia alizindua rasmi Siku ya Ziwa Victoria ambayo sasa itaadhimishwa kila mwaka tarehe 21 Mei katika nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.










Na Mwandishi Wetu,Michuzi TV

SHIRIKA la Umeme Tanzania(TANESCO)Mkoa wa Kinondoni Kusini jijini Dar es Salaam limewakumbusha wateja wake hasa wateja wakubwa kuhakikisha wanalipa ankra za umeme (bill)kwa wakati.

Akizungumza leo Mei 20,2026 katika kikao kati ya TANESCO Mkoa wa Kinondoni Kusini na Wateja Wakubwa  kilichokuwa na lengo la kujadiliana masuala mbalimbali Meneja wa TANESCO mkoa huo Adam Abdul ametumia bafasi hiyo kusisitiza ulipaji wa ankara za umeme kwa wakati ili kuwezesha shirika kuendelea kutoa huduma katika maeneo mengine.

“Tumekutana na Wateja Wakubwa katika mkoa wetu wa Kinondoni Kusini ,tumepokea changamoto zao na nyingi tumezifanyia kazi.Lakini nitumie nafasi hii kuwaambia wateja wetu wote walipe bill(Ankra)za umeme kwa wakati kwasababu zinapolipwa nasi zinatusaidia kufanya kazi na kuhakikisha upatikanaji wa umeme katika maeneo yote.”

“Kupitia kikao hiki wateja wetu wakubwa tumekubaliana wataendelea kulipa bill zao vizuri ,”amesema Abdull  na kufafanua pia  kwa sasa upatikani wa umeme umendelea kuimarika na hivyo kuondoa malalamiko kwa wateja wao.

Pia amesema kwa sasa TANESCO wanafanya kazi nzuri na malalamiko kwa wateja yamepungua na hata wateja wetu wakubwa katika kikao hawakuwa na malalamiko makubwa zaidi ya kuomba ankra kwa upande ziwahishwe ili nao walipe kwa wakati.

Kuhusu kikao cha TANESCO Kinondoni Kusini na Wateja Wakubwa,Abdull amesema kimekuwa na mafanikio makubwa na kwamba vikao vya namna hiyo ni endelevu kwani vinasaidia pande zote mbili kupata taarifa zenye lengo la kuboresha huduma.

Kwa upande wao baadhi ya wateja wakubwa waliohudhurika kikao hicho wametoa pongezi kwa TANESCO Mkoa wa Kinondoni Kusini kuandaa kikao ambacho kimewapa nafasi na kueleza yale ambayo wanaona yanakwenda kuboresha huduma za upatikanaji umeme . 








NA VICTOR MASANGU,KIBAHA

Chama cha mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kibaha mjini katika kutekeleza ilani kwa vitendo na kukiimarisha na  kukijenga chama  imeamua kufanya ziara  na sekretarieti  kwa  lengo la kuweza kukagua uhai wa chama hicho pamoja na jumuiya zake ikiwa sambamba na kupata fursa ya kufanya mikutano kwa ajili ya kuzungumza na wanachama wao.

Katika ziara hiyo ambayo inaongozwa na Katibu wa Chama cha mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kibaha mjini Issack Kalleiya pamoja na jopo la  sekretarieti ya chama hicho wameweza kushirikiana na viongozi mbali mbali wa Kata ya Kibaha na kujadili mambo mbali mbali ikiwemo suala ziama la uhai wa chama hicho.

Katibu huyo amesema kwamba wameamua kufanya ziara hiyo ya kupita katika kata mbali mbali na kukutana na wanachama wa ccm pamoja na viongozi wa kata  ya Kibaha ikiwa ni kuangalia mwenendo mzima wa uhai wa jumuiya zake leengo kubwa ikiwa ni kukiimarisha chama na kujijenga.

"Tupo katika ziara yetu nikiwa nimeambatana na wajumbe wa sekretarieti ya chama wakiwemo kuutoka jumuiya ya wazazi, jumuiya ya umoja wa wanawake, pamoja na jumuiya ya umoja umoja wa vijana lakini wote kwa pamoja ni kutembea na kuweza kujionea hali halisi ya jinsi uhai wa chama ulivvyo pamoja na uhai wa jumuiya zake kwa hivyo hilo ndilo kubwa la ziara yetu hii,"amebainisha Katibu Kalleiya.

Kalleiya amesema kwamba kwa sasa muda wa uchaguzi umeshamalizika kwa hivyo hakuna budi kushikamana kwa pamoja kati ya chama pamoja na kumuiya zake ili kuweza kujiandaa na chaguzi nyingine zinazokuja ndio maana wameona kuna umuhimu mkubwa wa kuwatembelea wanachama wao katika maeneo mbali mbali.

Ziara ya sekretarieti ya Chama  cha mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kibaha mjini imefanya ziara yake katika kata ya Kibaha pamoja na Kata ya Viziwaziwa ambapo lengo lake kubwa ni kutembea katika kata mbali mbali kwa ajili ya kuweza kuwatembelea wanachama wake pamoja na kuangalia suala zima la uhai wa chama jinsi ulivyo pamoja na kuweza kuangalia uhai wa jumuiya zake mbali mbali.



Na Janeth Raphael MichuziTv Bungeni Dodoma

-Serikali Yaeleza hatua Zinazoimarisha Ajira na Mazingira ya Kazi kwa Watumishi Wenye Ulemavu

Serikali imesema inaendelea kuimarisha utekelezaji wa sera, sheria na miongozo inayolenga kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata fursa sawa za ajira pamoja na mazingira rafiki ya kazi ndani ya Utumishi wa Umma na sekta binafsi nchini.

Kauli hiyo imetolewa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Regina Lowassa Qwaray wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Stella Ikupa Alex ambaye alihoji hatua iliyofikiwa na Serikali katika kutekeleza Mwongozo wa Ajira na Mazingira ya Kazi kwa Watumishi wenye Ulemavu katika taasisi za umma.

Akijibu swali hilo, Qwaray amesema Serikali imeweka msingi wa kisheria na kisera kupitia Sera ya Menejimenti na Ajira katika Utumishi wa Umma, Toleo la Pili la mwaka 2008 pamoja na Sheria ya Watu Wenye Ulemavu, Sura ya 183, ambazo zimeweka masharti mahsusi kuhusu ajira, haki za kazi na mazingira rafiki kwa watumishi wenye ulemavu katika Utumishi wa Umma na sekta binafsi.

Amesema katika kuhakikisha masharti hayo yanatekelezwa kwa vitendo, Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha ushirikishwaji wa watu wenye ulemavu katika maeneo ya kazi, ikiwemo kutungwa kwa Kanuni za Utumishi wa Umma za mwaka 2022 pamoja na Kanuni za Uendeshaji wa Shughuli za Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma za mwaka 2021.

Aidha, Serikali imeandaa Mwongozo wa Huduma kwa Watumishi wa Umma wenye Ulemavu wa mwaka 2008 ambao unalenga kusaidia taasisi za umma kuweka mazingira wezeshi na rafiki kwa watumishi wenye ulemavu ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi sawa na watumishi wengine.

Qwaray amesema miongoni mwa maeneo yanayopewa kipaumbele ni pamoja na kuhakikisha upatikanaji wa miundombinu fikivu katika maeneo ya kazi, huduma zinazozingatia mahitaji maalum ya watu wenye ulemavu pamoja na kuendelea kutoa elimu kwa taasisi mbalimbali kuhusu umuhimu wa usawa na ujumuishwaji mahali pa kazi.

“Serikali itaendelea kuweka misingi thabiti ya utekelezaji wa sera, sheria na miongozo kuhusu watumishi wenye ulemavu kwa kutoa elimu, kuhamasisha na kusimamia ujenzi wa miundombinu fikivu na rafiki kwa watu wenye ulemavu katika Utumishi wa Umma,” amesema Qwaray.

Ameongeza kuwa dhamira ya Serikali ni kuhakikisha mazingira ya kazi yanakuwa salama, jumuishi na yanayomwezesha kila mtumishi kutekeleza wajibu wake bila vikwazo vinavyotokana na hali ya ulemavu.

Hatua hizo zinaelezwa kuwa sehemu ya jitihada za Serikali za kuimarisha usawa wa kijamii, kuongeza fursa za ajira kwa watu wenye ulemavu na kuhakikisha haki zao zinazingatiwa katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku ndani ya taasisi za umma nchini.



Afisa Mtendaji Mkuu wa Yas Tanzania Bw.Pierre Canton-Bacara, akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa programu ya “Startups za Viwango” iliyofanyika hivi karibuni jijini Dar es Salaam. Mpango huo unalenga kusaidia 'startups' za Kitanzania kupita ushauri elekezi, mafunzo ya biashara, fursa za kufikia wawekezaji pamoja na mitandao ya kimkakati kibiashara. kushoto ni Bi. Hannah De Somviele, Meneja Mkuu wa Chemba ya Wafanyabiashara wa Ufaransa Tanzania (French Tanzania Chamber of Commerce)
Kampuni ya huduma za kidijitali na mawasiliano, Yas, kwa kushirikiana na Chemba ya Wafanyabiashara wa Ufaransa Tanzania (French Tanzania Chamber of Commerce), imezindua programu ya “Startups za Viwango”, mpango unaolenga kukuza kampuni changa za ubunifu nchini kupitia mafunzo, ushauri wa kitaalamu, fursa za uwekezaji pamoja na kuimarisha biashara.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa programu hiyo jijini Dar es Salaam, Afisa Mtendaji Mkuu wa Yas, Pierre Canton-Bacara, alisema mpango huo unalenga kusaidia vijana wabunifu kubadilisha mawazo yao kuwa biashara endelevu na zenye ushindani.

Alisema licha ya Tanzania kuwa na idadi kubwa ya vijana wenye ubunifu na mawazo yenye uwezo mkubwa wa kuleta mabadiliko, kampuni nyingi changa bado zinakabiliwa na changamoto za ukosefu wa ujuzi wa biashara, ufadhili na mwongozo wa kitaalamu.

“Kuna vijana wengi nchini wenye mawazo mazuri na suluhisho kwa jamii, lakini wengi wao hukosa mazingira sahihi ya kuyaendeleza na kuyakuza. Kupitia ‘Startups za Viwango’, tunataka kusaidia kuziba pengo hilo na kuwawezesha kufikia hatua kubwa zaidi,” alisema Canton-Bacara.

Aliongeza kuwa Yas inaendelea kuwekeza katika miundombinu ya kidijitali ili kuweka mazingira bora ya ukuaji wa biashara na ubunifu nchini.

“Ubunifu hauhitaji mtandao pekee, bali unahitaji mazingira yanayowezesha biashara kukua, kupata ushauri na kufikia masoko mapya. Ushirikiano huu unaonesha dhamira yetu ya kusaidia uchumi wa ubunifu nchini,” aliongeza.

Kupitia programu hiyo, kampuni changa zitapata mafunzo ya biashara, ushauri kutoka kwa wataalamu, nafasi za kukutana na wawekezaji pamoja na fursa za kuunganishwa na masoko ya kimataifa.

Sehemu ya programu hiyo ni pamoja na Yas Masterclass itakayotekelezwa kwa kushirikiana na Yas Business, ambapo wataalamu wa kampuni hiyo watashirikiana na waanzilishi wa startups kuimarisha mifumo yao ya biashara, mikakati ya ukuaji na uwezo wa kuvutia uwekezaji.

“Tunawaamini vijana wa Tanzania na tunaamini biashara wanazojenga zina uwezo wa kuzalisha ajira, kuchochea ukuaji wa sekta mbalimbali na kuiweka Tanzania katika nafasi nzuri ya ubunifu barani Afrika,” alisema.

Kwa upande wake, Meneja Mkuu wa Chemba ya Wafanyabiashara wa Ufaransa Tanzania, Bi. Hannah De Somviele, alisema ushirikiano huo una lengo la kuimarisha mazingira ya ubunifu nchini na kuzisaidia ‘startups’ za Tanzania kupata nafasi katika masoko ya kimataifa.

“Tunaamini wajasiriamali wa Tanzania wana uwezo mkubwa wa kushindana kimataifa. Kupitia programu hii, tunataka kuwapatia mitandao, mwongozo na fursa zitakazowawezesha kukuza biashara zao kwa kiwango cha kimataifa,” alisema De Somviele.

Na Mwandishi wetu, Ngorongoro.

Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa CRDB Bank Plc kutoka mataifa ya Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Falme za Kiarabu na Rwanda wamerejea Nyumbani Ngorongoro kushuhudia asili ya mababu zao iliyosheheni vivutio vya utalii vya Wanyamapori, Malikale, Urithi wa Utamaduni na Jiolojia vilivyopo Ngorongoro ambayo ni Kivutio bora cha Utalii Afrika mwaka 2023 na 2025.

Wakiwa ndani ya hifadhi hiyo maarufu duniani, Wakurugenzi hao  wamefurahishwa na mandhari, uoto wa asili, wanyamapori pamoja na huduma bora za utalii zinazotolewa ndani ya hifadhi na kusisitiza kuwa uzoefu walioupata umeacha alama inayowafanya kurudi tena na familia zao.

Akizungumza kwa niaba ya ujumbe huo, Mwenyekiti wa Bodi ya CRDB Prof. Neema Mori amesema ujumbe huo umeichagua Ngorongoro kuwa sehemu yao ya mapumziko kutokana na upekee wake usiofananishwa na eneo lolote duniani  kwa kuwa Ngorongoro si tu kivutio cha Utalii bali ni hazina ya historia, utamaduni na asili inayoishi.

Akiwa na Ujumbe huo Kamishna Msaidizi Mwandamizi anayesimamia Utalii na Masoko Mariam Kobelo amesema kuwa  Ngorongoro ndio eneo lenye ushahidi wa kisayansi na Kimazingira kuwa binadamu wa kwanza alisimama kwa miguu yake miwili zaidi ya miaka Milioni 3.6 iliyopita huku hifadhi hiyo ikipambwa na wanyama wakubwa watano "Big Five", Spishi za Wanyama mbalimbali, Ndege, maua na mimea.





Benki ya Exim Tanzania hii leo imezindua huduma yake ya Exim WhatsApp Banking, suluhisho jipya la kidijitali lililobuniwa kufanya huduma za kibenki za kila siku kuwa za haraka, rahisi na zinazofikika kwa kupitia jukwaa la WhatsApp.

Huduma hii inawawezesha wateja kupata huduma mbalimbali za kibenki moja kwa moja kupitia WhatsApp. Huduma hizo ni pamoja na kuangalia salio, kuhamisha fedha, kutuma fedha kwenda simu za mkononi, kufanya malipo kwa wafanyabiashara, kulipia huduma za serikali kupitia GePG, pamoja na huduma zinazohusiana na kadi za benki. Mteja anaweza kupata huduma zote hizi kupitia jukwaa la WhatsApp bila uhitaji wa kupakua programu nyingine yoyote wala haja ya kutembelea tawi la benki.

Mkuu wa Kitengo cha Mifumo Mbadala ya kidigitali wa Benki ya Exim, Bw Silas Matoi, akizungumza wakati wa uzinduzi, amesema mfumo huu umebuniwa kwa ajili ya kurahisisha upatikanaji wa huduma za kibenki na kuimarisha ubora wa huduma kwa wateja.

‘‘Kupitia Exim WhatsApp Banking, wateja wetu sasa wanaweza kuangalia salio kwenye akaunti zao, kutuma fedha kwenda kwenye mitandao ya simu, kulipa bili na malipo mbalimbali ya serikali, kupata huduma zote zinazohusiana na kadi, pamoja na kufanya miamala mingine moja kwa moja kupitia WhatsApp. Hii inaondoa ulazima wa aidha kupakua, kubadilisha programu mbalimbali au kupitia mifumo migumu, kwani sasa huduma zote muhimu za kibenki zinapatikana sehemu moja, iliyozoeleka, rahisi na inayopatikana kwa watu wote” Alisema Silas.

Katika hatua nyingine, bwana Matoi, ameeleza kuhusu ubora wa teknolojia iliyotumika kubuni mfumo huu na hakikisho la usalama.

“Tumejenga suluhisho hili huku tukizingatia misingi ya usalama na urahisi wake. Wateja wetu wasiwe na wasiwasi, wanaweza kufanya miamala kwa kujiamini wakijua kuwa kila mawasiliano yanalindwa kupitia mifumo salama ya uthibitishaji ikiwemo uthibitisho wa PIN. Wakati huo huo, mfumo huu unasalia kuwa rahisi, wa haraka na mwepesi kutumia, kwa sababu lengo kubwa ni kufanya huduma za benki kidijitali ziwe za kawaida na zinazofikika kwa kila mteja,” Amesema Matoi.

Huduma hii mpya ya Exim WhatsApp Banking, inawawezesha wateja wa Benki ya Exim kufanya miamala yao ya kila siku kupitia jukwaa hilo wanalolitumia kila siku, hivyo kuondoa ulazima wa kupakua aplikesheni nyingine tofauti huku wakifurahia huduma za kibenki zilizo rahisi, za haraka na zilizozoeleka.

Kwa upande wake Meneja Mkuu wa masoko na Mawasiliano wa Exim Benki Tanzania, Kauthar D’souza, akizungumzia umuhimu wa uzinduzi wa mfumo huu, amesema kuanzishwa kwa huduma ya Exim WhatsApp Banking kunadhihirisha dhamira endelevu ya benki hiyo katika kuleta ubunifu na kuboresha huduma kwa wateja.

“Wateja wetu tayari wanatumia WhatsApp kila siku kwa mawasiliano yao, kufanya biashara na kusimamia shughuli zao za kila siku. Kwa kuleta huduma za benki ndani ya mazingira hayo hayo, tunafanya huduma za kifedha kuwa rahisi kufikiwa, kueleweka na kutumika kwa urahisi zaidi. Mteja wetu hapaswi kujifunza mfumo mpya au kupakua aplikesheni nyingine ili tu kuangalia salio lako au kulipa bili. Huduma za benki zinapaswa kufanyika kulingana na namna unavyoishi na kufanya kazi, na si vinginevyo” Amesema Kauthar

“Uzinduzi huu ni sehemu ya mikakati yetu mipana ya kuendelea kuleta ubunifu unaochochewa na mahitaji halisi ya wateja wetu na kuendana na kasi ya mabadiliko ya teknolojia. Tunazingatia namna wateja wetu wanavyoishi, tunaelewa mifumo na majukwaa wanayoyaamini, na kisha tunabuni suluhisho rahisi linaloendana na maisha yao ya kila siku. Huduma ya Benki kupitia WhatsApp si tu njia mpya ya kutoa huduma, bali pia hatua inayodhihirisha kuwa benki ya Exim ni benki inayokua sambamba na wateja wake, inayosikiliza mahitaji yao, na kufanya maisha yao ya kifedha kuwa rahisi zaidi kila siku”

Wateja wanaweza kupata huduma hii kwa kuanzisha mawasiliano kwa njia ya ujumbe kupitia namba rasmi ya WhatsApp ya Benki ya Exim Tanzania [+255 675 800 100], ambapo wataelekezwa kupitia mchakato rahisi wa usajili ikiwemo kuweka PIN, kabla ya kuanza kutumia huduma mbalimbali zinazopatikana.

Benki ya Exim pia ina mpango wa kupanua huduma hii kwa kuongeza vipengele vingine ikiwemo maombi ya mikopo na huduma za uwekezaji, ikiwa ni sehemu ya mkakati wake endelevu wa mageuzi ya kidijitali.
Mkuu wa Kitengo cha Mifumo Mbadala ya kidigitali wa Benki ya Exim Silas Matoi (aliyekaa Kulia), akizungumza wakati wa uzinduzi wa mfumo Exim WhatsApp Banking unaolenga kuwawezesha wateja wa Benki ya Exim kupata huduma mbalimbali za kibenki ikiwamo kuangalia salio, kuhamisha fedha, kutuma fedha kwenda mitandao ya simu, kulipia bili na huduma za serikali, pamoja na huduma zinazohusiana na kadi za benki kupitia kupitia WhatsApp. Huduma hii ni sehemu ya mikakati ya benki hiyo kuleta ubunifu unaoendana na kasi ya mabadiliko ya teknolojia pamoja na uhalisia wa maisha ya kila siku ya wateja. Aliyekaa kushoto ni Meneja Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania, Kauthar D’souza. Uzinduzi huo umefanyika Mei 21, 2026 katika za makao makuu ya Benki ya Exim jijini Dar es Salaam.



MKUU wa Wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro, Kasilda Mgeni, ameisisitiza Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Wilayani humo kuendelea kubuni vyanzo vipya vya mapato pamoja na kuhamasisha matumizi ya mashine za kielektroniki za utoaji risiti (EFD) ili kulinda mapato ya serikali yasipotee.

Hayo ameyazungumza jana katika kikao cha Kamati ya Ushauri wa Kodi ya Wilaya ya Same ambapo alisema licha ya wilaya hiyo kufanya vizuri katika ukusanyaji wa mapato na kuvuka lengo lililowekwa, bado kuna umuhimu wa kuongeza jitihada katika kubuni vyanzo vipya vya mapato na kuimarisha matumizi ya mashine za EFD kwa wafanyabiashara wote.

“Tumefanya vizuri na kuvuka lengo la ukusanyaji wa mapato lililowekwa, lakini bado tuna wajibu wa kubuni vyanzo vipya vya mapato na kuendelea kuhamasisha matumizi ya mashine za EFD ili kuzuia upotevu wa fedha za serikali,” alisema Kasilda.

Aidha, aliwataka maafisa wa TRA kuwa karibu zaidi na wafanyabiashara pamoja na wananchi kwa kuwapa elimu ya mara kwa mara kuhusu umuhimu wa kulipa kodi kwa hiari na kuwasisitiza wananchi kudai risiti kila wanaponunua bidhaa au huduma mbalimbali.

Kwa upande wake Afisa wa TRA Wilaya ya Same, Angela Mwakaje, alisema kuwa taasisi hiyo imefanikiwa kukusanya zaidi ya shilingi bilioni 7.7 katika kipindi cha Julai 2025 hadi Aprili 2026, huku lengo lililowekwa likiwa ni shilingi bilioni 7.2.

Alieleza kuwa mafanikio hayo yameiwezesha TRA Same kufikia asilimia 107.5 ya makusanyo na hivyo kuvuka lengo lililopangwa.

Angela alisema mafanikio hayo yametokana na juhudi za kutoa elimu kwa walipakodi kuhusu umuhimu wa kulipa kodi kwa hiari pamoja na kuhamasisha wananchi kudai risiti kila wanaponunua bidhaa mbalimbali.

Kikao hicho cha Kamati ya Ushauri wa Kodi ni cha kisheria na hufanyika mara mbili kwa mwaka kwa lengo la kujadili mwenendo wa ukusanyaji wa mapato wilayani humo pamoja na kupendekeza mikakati bora ya kuhakikisha malengo ya mapato yanafikiwa. 


Top News