Na Mwandishi Wetu, WMTH – Dodoma

Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki (Mb), amesema Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari ili kuwawezesha wadau wa sekta ya sanaa kufanya kazi zao kwa ubora na tija.

Waziri Kairuki ameyasema hayo tarehe 14 Januari 2026, alipofanya mazungumzo na mtengeneza maudhui ya mtandaoni, Bw. Vicent Pendael Njau maarufu kama KIREDIO, aliyefika katika ofisi za Wizara hiyo zilizopo Mji wa Serikali Mtumba, Dodoma.

Katika mazungumzo hayo, masuala yaliyojadiliwa ni pamoja upatikanaji wa huduma ya intaneti ya uhakika, fursa za kujipatia kipato kupitia mitandao ya kijamii, pamoja na uwepo wa sera na mifumo ya kiserikali ikiwemo ya kikodi inayogusa sekta ya ubunifu na maudhui ya mtandaoni.

Waziri Kairuki alimpongeza Bw. Njau (Kiredio) kwa kazi nzuri anayofanya na kutoa wito kwa watengeneza maudhui pamoja na wasanii kwa ujumla kuzingatia maadili, mila na desturi za Kitanzania pindi wanapotengeneza maudhui yao na kabla ya kuyaweka mtandaoni.

Kwa upande wake, Kiredio ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwasikiliza vijana na kutambua mchango wao katika uchumi wa kidijitali, huku akiwasilisha changamoto mbalimbali zinazokabili sekta ya utengenezaji wa maudhui ili zifanyiwe kazi kwa wakati na kuiwezesha sekta hiyo kuendelea kukua.

Mazungumzo hayo yalihudhuriwa pia na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Bw. Mohammed Abdulla pamoja na baadhi ya Viongozi wa Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari.











Waswahili husema tembea uone na Mwenda bure si mkaa bure huenda ataokota.

Ukitaka kujaribu kuuokota mchanga unaohama njoo jirani na bonde la Olduvai ndani ya hifadhi ya Ngorongoro ushangae.

Jirani na bonde hili la Olduvai kuna mchanga unaohama ambao huwavutia mealfu ya watalii kuja kujionea maajabu hayo.

Mchanga huu upo katika umbo la nusu mwezi na upo karibu na Bonde la Olduvai ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro.

Mchanga huu wenye rangi nyeusi umetokana na madini ya chuma na majivu yaliyotokana na mlipuko wa Volcano kutoka Mlima Oldoinyo Lengai.

Mchanga huu ambao husogea kwa kasi ya takribani mita 15–29 kwa mwaka tuta lake lina urefu wa mita 5 na upana wa mita 100.

Hayo ndiyo maajabu ya Hifadhi ya Ngorongoro ukitaka kujua zaidi kuhusu mchanga huu tembea uone kwani fahari ya macho ni kuona na fahari ya macho haifilisi duka.

Tumerithishwa, Tuwarithishe.


Chama Cha Maafisa Mawasiliqno wa Serikali Tanzania (TAGCO) kimeendelea kutoa mafunzo mbalimbali ikiwemo matumizi ya teknolojia ya Akili unde (Artificial Intelligence – AI) kwa Maafisa Mawasiliano wa serikali kwa lengo la kuhakikisha wanafanya kazi kuendana na mabadiliko ya teknolojia.

Mafunzo hayo yanayoendeleq kufanyika Mkoa wa Morogoro yamejikita kuongeza ubunifu katika kazi na kuzifanya kuwa bora zaidi umaoendana na wakati.

Akizungumza katika mafunzo hayo, Mshauri Mwelekezi wa Mawasiliano ya Kimkakati Bi. Annastazia Rugaba, ameipongeza TAGCO kwa kuandaa mafunzo hayo, akisema kuwa ni hatua muhimu itakayowawezesha kuongeza weledi na ubunifu katika kazi zao za kiutendaji.

“Napenda nipongeze Chama Cha Maafisa Habari wa Serikali Tanzania (TAGCO) kwa kufanya mafunzo haya, ambayo naamini yataleta mabadiliko makubwa katika tasnia ya Mawasiliano kwa Umma. Kwanza, katika upande wa teknolojia nategemea tutapata mabadiliko chanya, kwa sababu fani hii ya Mawasiliano kwa Umma inategemea sana teknolojia. Hivyo ni lazima wajifunze ili waendane na mabadiliko ya teknolojia na kuweza kuweka utamaduni wa taasisi wa kujenga mawasiliano mazuri ndani na nje ya taasisi,” amesema Annastazia Rugaba

Kwa upande wake, Afisa Mawasiliano Mwandamizi kutoka Kampuni ya Uendelezaji Joto Ardhi Tanzania (TGDC) na mwanachama wa TAGCO, Boaz Mazigo, amesema amefurahishwa kuwa sehemu ya mafunzo hayo yanayowawezesha kutumia teknolojia ya akili mnemba katika kazi zao za kiofisi, akisema ni teknolojia inayosaidia kurahisisha na kuharakisha utendaji kazi.

“Ninayo furaha kubwa ya kuwa katika kikao hiki cha namna ya kutumia teknolojia ya akili mnemba, kwa sababu ni kitu ambacho kimekuja kutuletea mwanga mkubwa wa namna ambavyo kazi zetu zinapaswa kufanyika kwa ufanisi. Niwaombe viongozi wa taasisi nyingine waendelee kuwashika mkono Maafisa Habari ndani ya taasisi zao ili mafunzo kama haya yanapotangazwa nao waweze kushiriki,” Boaz Mazigo amesema

Naye Mkuu wa Kitengo cha Habari, kutoka Wizara ya Habari na Mawasiliano Zanzibar, Takdir Suweid, ametoa wito kwa waajiri katika sekta ya umma na binafsi kuwaruhusu wafanyakazi wao kushiriki mafunzo hayo ili kupata mabadiliko ya kiutendaji yatakayosaidia kuboresha utendaji wa kazi zao.


Na Mwandishi wetu, Simanjiro


WILAYA ya Simanjiro mkoani Manyara, imejipanga kuhakikisha inafanya mageuzi makubwa katika mazao ya kilimo na mifugo ili wakazi wa eneo hilo wapate tija zaidi na kunufaika kiuchumi.

Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro, mwalimu Fakii Raphael Lulandala ameeleza hayo kwenye kongamano la kilimo la mwaka 2025/2026 lililofanyika mji mdogo wa Orkesumet

Lulandala amesema Simanjiro ina maeneo makubwa ya kilimo na yenye rutuba ikiwemo ya umwagiliaji ila bado hayajatumika ipasavyo katika kulima, hivyo wahitaji wachangamkie fursa hiyo.

"Simanjiro imetenga kiasi cha hekta 17,000 kwa ajili ya kilimo ila hadi sasa zinatumia hekta 630 pekee kwa kulima, tunawakaribisha wakulima waje Simanjiro kwani tumejipanga kisawasawa maeneo ya kilimo yapo," amesema DC Lulandala.

Mkuu huyo wa wilaya ametaja baadhi ya mazao yanayostawi kwenye eneo hilo ni pamoja na mahindi, maharage, vitunguu, mpunga na ufuta.

Hata hivyo, amewaagiza maofisa ugani kuhakikisha wanahamia mashambani kwa lengo la kutoa elimu kwa wakulima na kutobakia maofisini kwao.

"Maofisa ugani ofisi zenu ziwe mashambani badala ya ofisini kwani waajiri wenu huwa wanapatikana mashambani hivyo tusikae maofisini kwetu," amesema DC Lulandala.

Mmoja kati ya wakulima katika wilaya hiyo Ibrahim Abdalah ameeleza kwamba kongamano hilo limekuwa na manufaa kwa wakulima kwani watakuwa na uhakika wa kupata pembejeo za kilimo kwa wakati tofauti na awali.

Abdalah amesema awali walinyanyasika mno kwa mbegu feki na wakulima kutopata mbegu zenye ubora hivyo kupata wakati mgumu kuvuna mazao ya maana ila kupitia kongamano hilo la mazao ya kilimo mbegu nyingi zenye ubora zimewafikia.

Bwana shamba mauzo wa kampuni ya mbegu ya Seedco Peter Timotheo ameeleza kwamba wamewajali wakulima wa Simanjiro kwa kuwapatia mbegu bora kwani mavuno bora huanza na mbegu bora.

Timotheo amewaasa wakulima wa wilaya ya Simanjiro kuhakikisha wanachangamkia fursa ya kuwepo kwa mbegu zao bora na kuzichukua ili wapate mavuno bora.



Na Mwandishi wetu, Dodoma.

Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) imeshiriki mkutano mkuu wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania kwa lengo la kunadi vivutio vya utalii na kuimarisha ushirikiano kati ya Ngorongoro na Mahakama.

Mkutano huo uliofunguliwa tarehe 13 januari, 2026 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan unaendelea hadi tarehe 16 Januari, 2026 ambapo wadau mbalimbali wa sekta ya sheria kutoka maeneo tofauti ya nchi wanashiriki kujadili masuala mbalimbali yanayohusu haki, utawala wa sheria na maendeleo ya mfumo wa utoaji haki nchini.

Ujumbe wa Ngorongoro uliongozwa na Kamishna msaidizi mwandamizi wa Uhifadhi anayesimamia idara ya utalii na Masoko Mariam Kobelo pamoja na Afisa Uhifadhi mwandamizi-Sheria Usaje Mwambene ambapo mada mbalimbali kuhusu vivutio vya utalii, fursa za uwekezaji, huduma zinazotolewa na upekee wa Ngorongoro kama kivutio bora cha utalii barani afrika kwa mwaka 2023 na 2025.

Aidha, NCAA imetumia mkutano huo kujenga uelewa kwa wadau wa sheria kuhusu misingi ya kisheria inayosimamia uhifadhi wa rasilimali za asili ili kutangaza vivutio mbalimbali vya utalii vinavyopatikana katika hifadhi hiyo ikiwemo Kreta za Ngorongoro, Empakai, Olmoti, maporomoko yaa maji endoro, Ndutu ambalo ni maarufu kwa mazalia ya nyumbu wanaaohama, mchanga unaohama, makumbusho ya olduvai, makumbusho na jiopaki na vingine vingi.








Na Pamela Mollel,Arusha.

Jiji la Arusha limeanza ukurasa mpya katika sekta ya bodaboda baada ya Mkuu wa Wilaya ya Arusha, Joseph Modest Mkude, kuzindua mradi wa kukopeshana pikipiki sambamba na mkakati wa kurahisisha upatikanaji wa leseni.

 Hatua hiyo inalenga kuwawezesha vijana kiuchumi na kubadili taswira ya bodaboda kutoka kelele za barabarani hadi ajira halali.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkude alisema bodaboda si tatizo, bali changamoto kubwa ni mfumo mgumu wa leseni na ukosefu wa usimamizi. 

Alisisitiza kuwa kufuata sheria za usalama barabarani ni wajibu, lakini serikali ina jukumu la kuweka mazingira rafiki kwa vijana wanaojitafutia kipato.

Katika kuwasaidia madereva wengi kuingia rasmi kwenye mfumo, DC Mkude alipendekeza mpango wa kugharamia leseni kwa pamoja, ambapo waendesha bodaboda watachangia nusu ya gharama huku wadau wakilipia nusu iliyobaki. 

Hata hivyo Madereva wametakiwa kujiandikisha ili mpango huo utekelezwe kwa uwazi na ufanisi.

Pia aliagiza Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Arusha kupunguza urasimu katika utoaji wa leseni, akisisitiza kuwa mafunzo ya siku moja yanatosha kwa madereva wanaoendesha kama biashara, badala ya kuwapeleka VETA kwa muda mrefu.

Pamoja na hatua hizo za kuwezesha, Mkude alisema operesheni dhidi ya pikipiki zitakazokiuka sheria zitaendelea, hasa kwa wahuni wanaosababisha fujo mitaani. Alisema dereva bodaboda anayejitambua hawezi kuhatarisha biashara yake kwa vitendo visivyo vya kistaarabu.

Kwa upande wa Umoja wa Waendesha Bodaboda Jiji la Arusha, mwenyekiti wake Shwahibu Hamisi alisema umoja huo umeanza mradi wa kukopeshana pikipiki kwa kushirikiana na kampuni ya TVS, ambapo pikipiki 20 tayari zimekopeshwa kwa awamu ya kwanza kwa fedha zilizochangwa.

Kwa ujumla, mradi huu unatajwa kuwa hatua muhimu katika kuwawezesha vijana wa Arusha, kupunguza ajali bara8barani na kuifanya bodaboda kuwa sekta rasmi yenye mustakabali mzuri wa kiuchumi na ajira.




Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma


Bunge la 13 limeunda jumla ya Kamati 17 huku wanawake wengi wakichomoza kuongoza kamati hizo, Wabunge wa upinzani wa Chaumma na ACT Wazalendo nao wapenya.

Majina ya vigogo yamechomoza kwenye Kamati hizo huku baadhi ya wabunge wakongwe wakirejea katika uongozi wa Kamati walizoongoza Bunge la 12.

Kamati zilizopewa wapinzani ni Hesabu za Serikali (PAC) ambayo amekabidhiwa Devotha Minja na Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) ambayo itaongozwa na Mbunge Tunduru Kaskazini Ado Shaibu.

Hii ni mara ya kwanza wapinzani kutoka vyama viwili tofauti wanaongoza Kamati hizo ambazo kwa kipindi kirefu zilikuwa chini ya Wabunge kutoka Chadema.

Katika taarifa ya Bunge, Devotha Minja atasaidiana Khalifan Aeshi ambaye amechaguliwa kuwa Makamu huku Kamati ya (LAAC) Makamu wake ni Abdallah Chikota.

Katika Bunge la 12 Kamati ya PAC iliongozwa na Naghenjwa Kaboyoka wakati Kamati ya LAAC Mwenyekiti wake alikuwa Halima Mdee wote wakitokea Chadema licha ya kuingia kwenye msukosuko wa kutimuliwa na chama chao.

Minja na Ado Shaibu wamepewa Kamati hizo ambazo zimekuwa na hoja nzito kutoka kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ambapo mara nyingi Mashirika na Halmashauri yametajwa kuwa na mapungufu ya mifumo ya kimanunuzi na kupelekea upotevu mkubwa wa fedha.

Kamati zingine zilizoundwa ni Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge ambayo Mwenyekiti wake ni Anne Kilango Malecela na Makamu wake ni Christina Mndeme huku Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Mwenyekiti ni Masanja Kadogosa na Makamu wake Dougras Masaburi.

Kamati ya Sheria ndogo itaongozwa na Cecilia Pareso na Makamu wake ni Yahya Zuberi lakini Kamati ya Utawala,Katiba na Sheria wamepewa wabobezi wa Sheria ambapo Mwenyekiti ni Dk Damas Ndumbaro na Makamu wake Edwin Swale.

Kamati ya Sheria ndogo itaongozwa na Cecilia Pareso na Makamu wake ni Yahya Zuberi lakini Kamati ya Utawala,Katiba na Sheria wamepewa wabobezi wa Sheria ambapo Mwenyekiti ni Dk Damas Ndumbaro na Makamu wake Edwin Swale.

Mashimba Ndaki ameendelea kuongoza Kamati ya Bajeti na Makamu wake ni Ally Hassan King.

Naibu Waziri wa Nishati wa zamani Subira Mgalu amechaguliwa Kamati ya Nishati na Madini akisaidiwa na Simoni Lusengekile.

Mbunge Mpanda Seleman Kakoso amerudi kwenye nafasi yake ya Mwenyekiti wa Kamati ya Miundombinu akisaidiana na Abubakari Asenga huku Kamati ya Afya na Masuala ya Ukimwi wamechaguliwa Dk Johannes Lukumay kuwa Mwenyekiti na Zeyana Abdallah Hamid ndiye Makamu.

Mbunge mwingine aliyerudia nafasi yake ni Timotheo Mzava ambaye ameendelea kuwa Mwenyekiti Kamati ya Ardhi,Maliasili na Utalii Makamu wake ni Mary Masanja na Kamati ya Elimu, Utamaduni na Michezo Husna Sekiboko atasaidiana na Cornel Magembe.

Kamati zingine ni Maji na Mazingira iliyorudi tena kwa Jackson Kiswaga nafasi ya Makamu ikienda kwa Profesa Pius Yanda na Kamati ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii itaongozwa na Hawa Machafu Makamu ni Regina Malima.

Aliyekuwa Mwenyekiti wa Bunge la 12 Nagma Giga safari hii amepewa kuongoza Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama Makamu ni Mbunge wa Dodoma Paschal Chinyele, Viwanda, Biashara, Biashara na Kilimo ameendelea Deodatus Mwanyika na Makamu wake amerudi Mariam Ditopile.

Kwenye Kamati ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) amechaguliwa Florence Kyombo atasaidiana na Jafari Chege.

Na. Joseph Mahumi na Saidina Msangi, WF, Dodoma.


Tanzania na Indonesia zimekubaliana kuendeleza zaidi ushirikiano wa kimaendeleo katika sekta mbalimbali za kiuchumi na kijamii ikiwemo kilimo na nishati kwa faida ya nchi hizo mbili.

Hayo yamebainishwa jijini Dodoma, baada ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omary (Mb), kukutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Indonesia nchini Tanzania, Mhe. Tri Yogo Jatmiko Avetisyan.

Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Balozi Omar, ameishukuru Serikali ya Indonesia kwa mchango wake mkubwa katika kusaidia sekta mbalimbali za uchumi wa Tanzania ikiwemo sekta za madini, kilimo na mifugo tangu kuanzishwa kwa uhusiano wa kidiplomasia mwaka 1964.

“Mwaka huu ni maadhimisho ya miaka 62 tangu kuanzishwa kwa uhusiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Indonesia, na uhusiano wetu umeendelea kuimarika zaidi kadiri miaka inavyosonga mbele, na pia tumeona ziara kati ya viongozi wetu Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alipotembelea Indonesia, na Mhe. Prabowo Subianto Rais wa Indonesia alipokuja Tanzania, hii ni ishara ya uhusiano thabiti unaojengwa juu ya heshima na ushirikiano wa kweli,” alisema Mhe. Balozi Omar.

Aidha, Mhe. Balozi Omar alisema kuwa, dhamira ya Indonesia katika kukuza maendeleo endelevu na kupunguza umasikini imechangia kubadilisha kwa kiasi kikubwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini Tanzania kupitia misaada ya kifedha, ushauri wa kitaalamu, na programu za kujenga uwezo.

Aidha Mhe. Balozi Omary aliwaalika wawekezaji kutoka Indonesia kuja kuwekeza nchini katika sekta mbalimbali za kiuchumi na kijamii ikiwemo kilimo, uongezaji thamani wa mazao, madini, viwanda, nishati, miundombinu, afya, elimu na utalii.

Kwa upande wake, Balozi wa Indonesia nchini Tanzania, Mhe. Tri Yogo Jatmiko Avetisyan, alisema kuwa katika kuhakikisha kuwa nchi hizo zinadumisha ushirikiano zaidi ya Watanzania 170 wamepata manufaa kupitia programu hizo za kujenga uwezo katika sekta mbalimbali ikiwemo kilimo, mifugo, nishati, madini, uvuvi na fedha.

“Tutahakikisha tunaimarisha zaidi uhusiano huu kwa kuongeza kuwajengea uwezo wataalmu wa Tanzania ili maeneo yote tuliyokubaliana kushirikiana yanaleta tija na ustawi mpana wa uhusiano wa nchi hizi mbili,” alisema Mhe. Balozi Avetisyan.

Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Bi. Amina Khamis Shaaban, Naibu Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango, Dkt. Blandina Kilama, Kamishna wa Idara ya Fedha za Nje Wizara ya Fedha, Bw. Rished Bade, Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Bi. Tiba Kisonga na maafisa wengine waandamizi kutoka Wizara ya Fedha na ubalozi wa Indonesia nchini.


Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akimkabidhi Balozi wa Indonesia nchini Tanzania, Mhe. Balozi Tri Yogo Jatmiko Avetisyan, zawadi iliyokuwa na bidhaa zinazozalishwa nchini Tanzania ikiwemo korosho na kahawa, baada kikao walipokutana na kufanya mazungumzo, katika ukumbi wa mikutano wa Waziri wa Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.


Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akisalimiana na Balozi wa Indonesia nchini Tanzania, Mhe. Balozi Tri Yogo Jatmiko Avetisyan, walipokutana na kufanya mazungumzo, katika ukumbi wa mikutano wa Waziri wa Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.




Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akizungumza wakati wa kikao na Balozi wa Indonesia nchini Tanzania, Mhe. Balozi Tri Yogo Jatmiko Avetisyan, alipofika kwa ajili ya mazungumzo, katika ukumbi wa mikutano wa Waziri wa Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.


Waziri wa Fedha wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akiongoza kikao cha mazungumzo na Balozi wa Indonesia nchini Tanzania, Mhe. Balozi Tri Yogo Jatmiko Avetisyan, ambaye alifika kwa ajili ya mazungumzo, katika ukumbi wa mikutano wa Waziri wa Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.


Balozi wa Indonesia nchini Tanzania, Mhe. Balozi Tri Yogo Jatmiko Avetisyan, akizungumza katika kikao na Waziri wa Fedha Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), walipokutana na kufanya mazungumzo, katika ukumbi wa mikutano wa Waziri wa Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma.


Waziri wa Fedha wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (wa nne kulia), na Balozi wa Indonesia nchini Tanzania, Mhe. Balozi Tri Yogo Jatmiko Avetisyan (wa tano kulia), wakiwa katika picha ya pamoja na Viongozi na Wataalamu kutoka Wizara ya Fedha, Tume ya Mipango na Ubalozi wa Indonesia, baada ya kikao cha mazungumzo kilichofanyika katika ukumbi wa Waziri wa Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma. Kutoka kushoto Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Bi. Tiba Kisonga, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Bi. Amina Khamis Shaaban na Kamishna wa Idara ya Fedha za Nje Wizara ya Fedha, Bw. Rished Bade. Kutoka kulia ni Katibu wa Balozi wa Indonesia Bw. Antidius Karoli Kalisa, Mkuu wa Idara ya Utamaduni, siasa na Mambo ya Kijamii Bw. Michael Bastian Supit na Naibu Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango, Dkt. Blandina Kilama,



(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Dodoma)

Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma.

Waziri wa Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa amewataka wadau wote wanaosimamia ujenzi wa Kiwanja cha ndege cha Kimataifa cha Msalato kushirikiana ili ujenzi huo ukamilike ifikapo Mwezi Mei mwaka huu.

Akizungumza jijini Dodoma, Januari 14, 2026 wakati akikagua maendeleo ya ujenzi huo, Prof. Mbarawa amesema hatua ya ukamilishaji wa ujenzi (finishing), inahitaji umakini, kujali thamani ya fedha na ubora wa vifaa unaoendana na mahitaji.

"Mameneja wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), Mamalaka ya Viwanja vya ndege (TAA), Mamlaka ya Usafiri wa Anga (TCAA) pamoja na Zimamoto na Uhamimiaji shirikianeni kikamilifu ili vifaa na mifumo ya uendeshaji isomane na kurahisisha utendaji wa kazi kiwanjani hapo", amesisitiza Prof. Mbarawa.

Kwa upande wake, Meneja wa TANROADS mkoa wa Dodoma Eng. Zuhura Amani amesema wamejipanga kumsimamia kikamilifu mkandarasi anaejenga kiwanja hicho ili kikamilike kwa wakati.

Nae, Mkurugenzi wa Kiwanja kiwanja hicho, Clemence Mbaruck amesema watahakikisha ujenzi unakamilika kwa viwango na tayari watumishi 170 tayari wameshahamishiwa Dodoma kwaajili ya kuanza kazi kwenye kiwanja hicho mara baada ya kufunguliwa rasmi.

Zaidi ya shillingi bilioni 370 zinatumika kwaajili wa ujenzi huo na kukamilika kwake kutachochea ukuaji wa uchumi kwa wakazi wa Dodoma kwani kutaruhusu ndege aina mbalimbali za kitaifa na kimataifa kutua Kiwanjani hapo.





WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amekutana na Balozi wa Japan nchini Tanzania Mhe. Yoichi Mikami na kujadiliana naye masuala ya uchumi, miradi ya maendeleo na uwekezaji.

Akizungumza na Balozi huyo leo (Jumatano, Januari 14, 2026) ofisini kwake Mlimwa jijini Dodoma, Waziri Mkuu ameishukuru nchi hiyo kwa kuendelea kushirikiana na Tanzania kukamilisha ujenzi wa miradi mbalimbali kama vile barabara ya Arusha hadi Holili, bandari ya Kigoma, miradi ya kilimo na upatikanaji wa vifaa tiba vya huduma za afya ya mama na mtoto.

“Serikali itahakikisha kuwa miradi hii inatekelezwa kwa ufanisi mkubwa na inakamilishwa kama ilivyopangwa,” amesema Dkt. Mwigulu 

Dkt. Mwigulu ametumia fursa hiyo kutuma salamu za pongezi kwa Waziri Mkuu wa Japan, Bibi Sanae Takaichi kwa kuteuliwa kushika nafasi hiyo tangu Oktoba, 2025 na kuweka historia ya kuwa mwanamke wa kwanza kushika wadhifa huo nchini humo. “Tanzania inasisitiza kuendeleza ushirikiano wa karibu na Japan kwa manufaa ya pande zote mbili,” amesema.

Kwa upande wake, Balozi Mikami alimweleza Waziri Mkuu kwamba amefurahishwa na kasi ya utekelezaji wa miradi ya kijamii 79 ambayo awali ilikuwa inasuasua na kwamba tangu Septemba, 2024 hadi sasa, imebakia miradi 16 tu.

Alisema nchi yake itaendeleza ushirikiano na Tanzania ambao umedumu kwa miaka zaidi ya 60. 







WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amezitaka wizara zinazohusika na masuala ya ajira zisimamie kikamilifu utekelezaji wa sheria zinazotaka kazi zinazoweza kufanywa na Watanzania zisifanywe na wageni isipokuwa zile zinazohitaji utaalamu ambao nchi inaupungufu.

 Vilevile, Waziri Mkuu amekemea tabia ya baadhi ya wenye nyumba kumpangisha raia mmoja wa kigeni na kumruhusu mpangaji huyo apangishe watu wengine ndani ya nyumba hiyo jambo ambalo ni hatari kwa usalama na pia halina tija kibiashara.

Mheshimiwa Dkt. Mwigulu ametoa agizo hilo leo Jumatano, Januari 14, 2026 alipofungua Kikao cha Mawaziri, Naibu Mawaziri, Makatibu Wakuu na Manaibu Makatibu Wakuu wa Wizara za Kisekta kujadili fursa za ajira ndani na nje ya nchi.

Agizo hilo linalenga kuongeza fursa za ajira kwa Watanzania kufuatia kuwepo kwa wimbi kubwa la wageni kufanya kazi au biashara ambazo zinaweza kufanywa na Watanzania na kuliwezesha Taifa kukabiliana na changamoto ya upungufu wa ajira.

“…Kazi zinazoweza kufanywa na Watanzania ziachwe wafanye, si kuruhusu wageni wafanye. Tusioneane aibu kama tumefungua milango au kulegeza wataalamu wafuatilie. Wageni wafanye kazi za kitaalamu ambazo nchi ina uhaba wa wataalamu.”

 Amesema kuwa ni lazima wataalamu wa ndani wasimamie sheria ipasavyo na kama kuna maeneo yanayokwamisha wayabainishe na yafanyiwe marekebisho. “Hatuwezi kuleta watu wanaokuja kufanya kazi ambazo Watazania wanaziweza.” 

Katika hatua nyingine, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu ametoa wito kwa Watanzania kuwa na wivu na nchi yao kwa kutoruhusu baadhi ya vitu kufanyika, ambapo alitolea mfano suala la wenye nyumba kumpangisha raia moja wa kigeni ambaye naye analeta wenzake wengi katika nyumba hiyo hiyo.

“Watanzania tuwe na wivu na nchi yetu, mfano mtu anamkodishia nyumba mgeni kwa dola 5,000 kwa mwaka na kisha mgeni huyo anawaleta wenzake 60 na anawakodisha dola 500 hapo Mtanzania anapata hasara, hii si sawa hata kwa usalama.”

Waziri Mkuu amewaagiza wahusika wafuatilie suala hilo la makazi ili wakae katika utaratibu ulio rasmi. “Eneo hili liangaliwe wageni wanalundikana na kufanya kazi ambazo Watanzania wangeweza kufanya, hatuwezi kuruhusu hili tunataka wawekezaji.”

Hivyo, Waziri Mkuu ameziagiza wizara zinazohusika zifuatilie suala hilo, pamoja na kuwasisitiza wasimamie utekelezwaji wa sheria kwa sababu kila nchi ina sheria zake na Tanzania inatekeleza majukumu yake kwa kufuata sheria.

Amesema sheria zimetungwa ili kusaidia kujenga kampuni za Watanzania na kuzikuza, hivyo wizara zinazohusika zihakikishe hazisajili kampuni za kigeni kabla ya kuzifanyia uchunguzi wa kina kwa sababu baadhi ya taarifa zinazowasilishwa si sahihi.







Kasoko ya Empakaai ni mojawapo ya Kasoko za volkano ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro, ikiwa na kingo za juu na ziwa zuri linalofunika zaidi ya asilimia 75 ya sakafu ya Kreta/Kasoko. Kivutio kikubwa ndani ya kreta hii ni idadi kubwa ya ndege heroe (flamingo) wanaoonekana kando ya ufukwe wa ziwa, Ndege wanapokuwa wengi hufanya ziwa hilo kuwa na rangi ya pinki.

Kreta hii katika nyanda za juu za Ngorongoro imezungukwa na kuta za misitu yenye mteremko mkali wa takribani mita 300 kwa urefu, zikiwa na uoto wa asili wa kijani kibichi, wanyamapori na aina mbalimbali ya ndege. Eneo lake lina upana wa takribani kilomita 8, huku karibu nusu ya sakafu yake ikifunikwa na ziwa la lenye magadi na kina kirefu, makazi ya heroe (flamingo) na ndege wengine wa majini. 

Kutoka juu ya ukingo wa kreta ya Empakai, wageni wanaweza kuona Mlima Oldoinyo Lengai, Bonde la Ufa na Ziwa Natron kwa mandhari ya kuvutia. Pia wanaweza kufurahia matembezi ya asili kutoka juu ya mlima au kushuka hadi sakafuni kushuhudia vivutio vilivyopo.

Empakaai ina kimo cha takribani mita 3,200 kutoka juu ya usawa wa bahari upande wa magharibi na mita 2,590 upande wa mashariki. Mara nyingi hufunikwa na ukungu kutokana na mwinuko wake ambapo ziwa huonekana la kijani kibichi au buluu ya kina.

Kreta/Kasoko  ya Empakaai ni maarufu kwa safari za kutembea kwa miguu, ambapo watalii hutembea kwa takribani saa mbili na nusu kwenda na kurudi kutegemea na uwezo wa mwili. Wageni wanaweza kuona kwa ukaribu ziwa na msitu mnene uliopo ndani na kuzunguka sakafu ya Kasoko.

 Kivutio cha Empakaai kinaweza kutembelewa wakati wowote wa majira ya mwaka, lakini inapendelewa zaidi kuanzia mwezi Juni hadi Desemba (msimu wa kiangazi).

 _Karibu Ngorongoro 

Tumerithishwa, tuwarithishe_ 








Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Japan nchini Tanzania Mhe. Mikami Yoichi, mazungumzo yaliyofanyika Ikulu Chamwino mkoani Dodoma, leo tarehe 14 Januari 2025.

Mazungumzo hayo yamelenga kuimarisha zaidi ushirikiano uliopo baina ya Tanzania na Japan.





 


Top News