Na WMJJWM – Geita. 

Wanawake wachimbaji madini Mkoani Geita wamehimizwa kutumia fursa za mikopo inayotolewa na Serikali kupitia benki ya NMB ili kukuza na kuinua shughuli zao za uchimbaji na biashara zinazohusiana na sekta ya madini.

Wito huo umetolewa leo Machi 07, 2026, Mkoani humo na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. John Jingu wakati akizungumza katika kongamano la wanawake wachimbaji madini lililofanyika mkoani Geita.

Dkt. Jingu amesema Serikali imeweka mazingira rafiki ya kuwawezesha wanawake kiuchumi kupitia mikopo na mafunzo ya ujasiriamali, na kuwataka wanawake wachimbaji madini kujitokeza kuomba mikopo hiyo ili kuimarisha shughuli zao na kuongeza tija katika sekta ya madini.

Amesema wanawake ni uti wa mgongo wa familia, jamii na Taifa, hivyo wanapowezeshwa kiuchumi familia zao hupata maendeleo na ustawi.

“Serikali ipo tayari kusaidia wachimbaji madini, hususan wanawake, ili waweze kunufaika na fursa zilizopo katika sekta ya madini na kuchangia zaidi katika ukuaji wa uchumi,” amesema Dkt. Jingu.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Chama cha Wanawake Wachimbaji Madini, Salma Ernest amesema chama hicho kimekuwa kikitoa mchango mkubwa katika huduma za kijamii nchini.

salam amesema kupitia chama hicho wamefanikiwa kusaidia miradi mbalimbali ikiwemo ujenzi wa shule mkoani Tanga pamoja na kutoa huduma mbalimbali za kijamii kwa wafungwa katika baadhi ya magereza nchini.

Aidha amesema chama hicho kinaendelea kuwawezesha wanawake wachimbaji madini kwa kuwapa elimu ya fedha, kuwahamasisha kuanzisha miradi ya pamoja na kukuza shughuli zao za kiuchumi ili waweze kujikwamua kiuchumi na kuchangia maendeleo ya jamii.


📌Atoa maelekezo mahsusi kwa Mkandarasi na Wasimamizi wa mradi

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe.Salome Makamba leo amekagua utekelezaji wa mradi wa kuzalisha umeme wa Malagarasi (MW 49.5) unaotekelezwa katika Wilaya ya Uvinza mkoani Kigoma ambapo ameeleza kutoridhishwa kwake na kasi ya utekelezaji.

Akiwa katika Kijiji cha Mazungwe wilayani Uvinza Mhe Salome amekagua sehemu mbalimbali za mradi ikiwemo ujenzi wa tuta na uchepushaji mto, ujenzi wa jengo la kuendeshea  mitambo na kambi za wafanyakazi ambapo hakukuta wafanyakazi wa kutosha kama ambavyo mkataba unaelekeza.

Kutokana na hilo, Naibu Waziri wa Nishati amemuagiza mkandarasi kampuni ya Dongfang ya China kuhakikisha kuwa anaongeza wafanyakazi,  vifaa vya kazi na ndani ya mwezi mmoia awe amejenga kambi ya wafanyakazi.

Aidha,  amemtaka Mkandarasi kuwasilisha ratiba mpya  ya utekelezaji wa kazi.

Vilevile, ameagiza wasimamizi wa mradi wa Malagarasi kutoka Kampuni ya Mkandarasi  Mshaurii na TANESCO kuhamia katika eneo la mradi ndani ya mwezi  mmoja ili kuweza kuusimamia mradi huo kwa ukaribu.

"Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameiagiza Wizara ya Nishati kuzalisha megawati 8000 za umeme ifikapo 2030, hatutakubali mtu atukwamishe katika kufikia malengo haya. Mkandarasi hakikisha unakamilisha kazi ifikapo Oktoba 2027 kama mkataba unavyoelekeza." Amesisitiza Mhe.Salome

Aidha, amemtaka Mkandarasi  Mshauri kampuni ya Multiconsult Norge AS ya Norway na Norplan kutoka Tanzania kuhakikisha kuwa wanamsimamia mkandarasi ipasavyo ili mradi ukamilike kwa wakati na kwa viwango stahiki.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Dinah Mathamani ameeleza kuwa uongozi wa wilaya hiyo utasimamia kwa karibu maelekezo yanayotolewa na Wizara ili mkandarasi atekeleze kazi kulingana na.mkataba.

Naye, Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati (Umeme na Nishati Jadidifu), Mhandisi Edson Ngabo amesema utekelezaji wa mradi wa Malagarasi kwa saaa ulipaswa kuwa kwenye asilimia 28 ila  umefikia asilimia 23.

Amesema Wizara ya Nishati itaendelea  kumsimamia kwa karibu mkandarasi  ili amalize kazi kwa wakati.

Sehemu nyingne zinazohusisha mradi wa Malagarasi ni upelekaji umeme katika vijiji saba vyenye vitongoji 18 ambapo mradi huo umekamilika kwa asilimia 100.

Pia ujenzi wa njia ya msongo wa kV 132 kutoka eneo la mradi hadi Kidahwe ambao umekamilika kwa asilimia 100.





Mwasisi wa Chama Cha Wanahabari Wanawake Tanzania(TAMWA),Fatma Aloo akizungumza wakati wa Iftari iliyofanyika katika Ofisi za TAMWA jijini Dar es Salkaam kwa kuunganisha Waandishi wa habari wakongwe na wakati na wasasa. Iftaru hiyo imefanyika Machi 06, 2026.


CHAMA cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania, Tanzania Media Women’s Association (TAMWA), kimesisitiza umuhimu wa kuendeleza harakati za kupigania haki za wanawake na watoto huku kikikumbusha historia ya kuanzishwa kwa harakati hizo na mchango wake katika kupambana na dhuluma za kijinsia nchini.

Akizungumza katika Iftari iliyofanyika Machi 06, 2026 ikiwa ni kuelekea maadhimisho ya miaka 37 tangu kuanzishwa kwa TAMWA, mmoja wa waanzilishi wa chama hicho, Fatma Alloo, alisema harakati za kutetea haki za wanawake zilianza muda mrefu na bado zina umuhimu mkubwa hadi leo kutokana na changamoto zinazoendelea kujitokeza.

Alieleza kuwa TAMWA ilianzishwa siku ya maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, wakati huo ikiwa ni kundi dogo la waandishi wanawake waliokuwa wakifanya kazi kwa karibu na gazeti la Daily News, wakilenga kuibua masuala ya kijinsia katika jamii.

Fatma alisema wakati wanaanzisha harakati hizo walikuwa bado vijana na hawakuwa na uelewa mpana wa aina zote za dhuluma, lakini walikuwa wanashuhudia mateso na changamoto zilizokuwa zikiwakumba wanawake na watoto katika jamii.

Alisisitiza kuwa licha ya jitihada zilizofanyika kwa miaka mingi, dhuluma dhidi ya wanawake bado ipo na hata inaonekana katika baadhi ya nchi zilizoendelea barani Ulaya, jambo linaloonesha kuwa mapambano hayo yanahitaji kuendelea kupewa kipaumbele na vizazi vijavyo.

Pia alisema kwa kusema Wakati wameanza harakati za kuanzisha TAMWA, waume zao walikuwa wakituwaunga mkono  na hiyo waliwatia nguvu zaidi, ili kuendeleza mapambano ya dhuluma kwa wanawake  na watoto.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Dkt. Rose Reuben, alisema mkutano huo umeandaliwa mahsusi kukusanya na kuhifadhi hadithi na historia ya kazi zilizofanywa na wanachama wa chama hicho katika kutetea haki za binadamu kwa mtazamo wa kijinsia.

Alieleza kuwa pamoja na kukusanya historia, mkutano huo pia unalenga kutambua na kuheshimu mchango wa wanachama waliotoa Kwa muda, nguvu na maarifa yao katika kuimarisha harakati za kupigania haki za wanawake, wakiwemo wale waliotangulia mbele ya haki.

Aidha, TAMWA ilibainisha kuwa katika mafanikio yake, chama hicho kimefanikiwa kupata shamba lenye ukubwa wa takribani hekta 98 ambalo linatarajiwa kusaidia kuendeleza shughuli na miradi ya shirika hilo kwa lengo la kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia.

Chama hicho pia kimeonya kuwa pamoja na uwepo wa sera na sheria mbalimbali za kulinda haki za wanawake na watoto wa kike, bado kuna changamoto kubwa katika utekelezaji wake, hasa kutokana na mabadiliko ya kijamii na kuongezeka kwa vitendo vya ukatili kupitia mitandao ya kijamii.

Kutokana na hali hiyo, TAMWA imevitaka vyombo vya habari, mamlaka za mawasiliano na wadau wengine kushirikiana kikamilifu katika kupambana na ukatili wa kijinsia, hususan unaofanyika mitandaoni, huku jamii ikihimizwa kuacha kuvumilia vitendo hivyo na kulinda watoto dhidi ya mazingira hatarishi.
Tanzania imeungana na Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Nchi za Ukanda wa Bahari ya Hindi (IORA) kuadhimisha miaka 29 ya kuanzishwa kwa jumuiya hiyo katika hafla iliyofanyika katika mji wa Serikali, Mtumba jijini Dodoma ambapo miti ya Matunda na Kivuli imepandwa.

Akiongoza maadhimisho hayo, Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais anayeshughulikia Mazingira Balozi Baraka Luvanda ameshiriki mazoezi mepesi na upandaji miti ya matunda na kivuli uliofanyika katika Ofisi za Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ikiwa ni ishara ya utunzaji wa mazingira na kuimarisha afya za washiriki.

Akizungumza katika maadhimisho hayo, Balozi Luvanda ameeleza namna nchi inavyonufaika na IORA kupitia Jitihada za pamoja za kuhakikisha rasilimali za Bahari ya Hindi zinatumika kwa maendeleo endelevu na kuongeza kuwa Jumuiya hiyo inawawezesha nchi wanachama kukusanya nguvu na kukabiliana na changamoto mbalimbali kwa pamoja.

Pia ameeleza kuwa kupitia jumuiya hiyo nchi wanachama zimekuwa zikipambana na uvuvi haramu, kutangaza fursa zinazopatikana katika bahari ya Hindi hususani uchumi wa buluu, kubadilishana uzoefu na kujengeana uwezo kwa watalaam wa nchi wananchama na kutoa wito kwa wadau kuendelea kushiriki kikamilifu katika shughuli za IORA na kuchangamkia fursa mbalimbali zinazopatikana ndani ya Jumuiya hiyo.

Ameeleza kuwa zoezi la upandaji miti lililofanyika linaunga mkono maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia kampeni ya “27 ya Kijani”.

“Hii pia ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje ya mwaka 2001 (Toleo la 2024) na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambazo kwa pamoja zinatilia mkazo uhifadhi wa mazingira na ustahimilivu dhidi ya changamoto za kiikolojia,” alisisitiza Balozi Luvanda.

Maadhimisho hayo yamefanyika chini ya kauli mbiu isemayo “IORA INABORESHA MAISHA” (IORA Improves Lives), ikilenga kuongeza uelewa wa umma kuhusu umuhimu wa Jumuiya hiyo kwa jamii za nchi wanachama.








VICTOR MASANGU,KIBAHA

Wafanyakazi wanawake wa kampuni ya SF group ya Jijini Dar es Salaam katika kuadhimisha maadhimisho ya siku ya mwananke duniani wameamua kutoa msaada wa vitu mbali mbali katika shule ya Sekondari Koka pamoja na kufanya matendo ya huruma katika vituo viwili vya kulelea watoto yatima vilivyopo Katika Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha.

Katika kuona umuhimu wa siku hiyo wanawake hao wa kampuni ya SF group katika kukuza sekta ya elimu wameweza kutembelewa wanafunzi wanaosoma katika shule ya Koka sekondari iliyopo katika kata ya Sofu na kutoa msaada wa vitu mbali mbali ikiwemo kompyuta tatu, madaftari, pamoja na taulo za kike ambazo zitakuwa ni mkombozi mkubwa kwa wanafunzi wa kike.

Akizungumza katika sherhe za maadhimisho hayo ambayo yamefanyika katika Jimbo la Kibaha mjini Mkurugenzi wa Rasirimali watu na utawala wa kampuni ya SF Group Marygoreth Faustine ambaye aliongoza na kundi la wanawake kutoka makampuni mbali mbali yaliyopo ndani ya Sf Group amesema kwamba dhamira yao kubwa ni kurudisha fadhila kwa jamii ikiwa sambamba na kusaidia kuinua sekta ya elimu na afya.

"Sisi kama wanawake wa SF Group tumeamua kuitumia siku hii ya kipekee ya maadhimisho ya mwananke duniania kwenda kutembelea baadhi ya maeneo yaliyopo katika Jimbo la Kibha mjini na kwamba tumetoa msaada wa vitu mbali mbali katika shule ya Koka sekondari ikiwemo Kompyuta tatu, taulo za kike, pamoja na madaftari na mahitaji mengine ya msingi ambayo yataweza kuwasaidia wanafunzi katika kuongeza kiwango cha ufaulu," amesema Mariagoreth.

Pia Mkurugenzi huyo amebainisha kwamba katika ziara hiyo wameweza kupata fursa ya kutembelea Zahanati ya Mwendapole na kutoa msaada wa mahitaji mbali mbali katika wodi ya wakinamama na kuwakabidhi msaada wa vifaaa mbali mbali ambayo vitawasaidia wakinamama wajawazito pamoja na wale ambao tayari wameshajifungua.

“Tumeungana kwa pamoja na wanawake wote wa kampuni ya SF Group katika kusherekea maadhimisho ya kilele cha siku ya wanawake duniani kwa kimsingi tumeweza kupata fursa ya kutembelea katika maeneo manne ambapo pia tumefanya matendo ya huruma katika vituo vya watoto yatima," amebainisha Mkurugenzi Mariagoleth.

Pamoja na hayo walikwenda kutembelea kituo cha watoto yatima cha Fadhila kilichopo kata ya misugusugu pamoja na kituo kingine cha Shalom kilichopo kata ya Msangani na kufanya matendo ya huruma na kutoa msaada wa mahitaji mbali mbali ikiwemo sabuni, sukari, unga, mafuta, sabuni za kufulia na kuogea, dawa za meno pamoja na vitu vingine vya msingi ambavyo vitaweza kuwasaidia wattoto hao.

Katika hatua Mkurugenzi huyo amebainisha kwamba lengo kubwa la kwenda kutoa msaada katika maeneo mbali mbali ya Jimbo la Kibaha mjini ni kwa ajili kuonyesha ushirikiano wa pamoja kati yao na jamii amabayo inawazunguka ikiwa pamoja na kuunga mkono juhudi za serikali katika kuleta chachu ya maendeleo na kuisaidia jamii katika mambo mbali mbali ikiwemo afya, elimu, pamoja na huduma za kijamii.

Naye mwalimu mkuu wa shule ya Koka Sekondari Magreth William aliwashukuru kwa dhati wanawake hao wa kampuni ya SF Group kwa msaada huo ambao wameutoa pamoja na kumshukuru kwa dhati Mbunge wa Jimbo la Kibaha mjini Silvestry Koka kwa kutoa sapoti kubwa katika kuboresha sekta ya elimu katika maeneo mbali mbali ikiwemo shule hiyo ya Koka sekondari.

Nao baadhi ya watoto yatima na wanaoishi katika mazingira magumu katika vituo vya Fadhila na Shalom wametoa shukrani zao za dhati kwa wanawake wa kampuni hiyo ya SF Group kwa msaada huo kutoka kwa wanawake wa SF Group.

Wanawake wa kampuni ya SF Group wametumia kilele cha maadhimisho ya siku ya mwanamke duniani kufanya matendo ya Huruma katika sehemu nne ikiwemo kituo cha watoto yatima cha Fadhila, Shalom, zahanati ya Mwendapole pamoja na kutoa msaada katika shule ya Koka sekondari.






















Balozi wa Tanzania nchini Zimbabwe, Kamishna wa Polisi (CP) Mhe. Suzan Kaganda, amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Ethiopia nchini Zimbabwe, Mhe. Rashid Mohammed Abdulwahid, ambapo wamejadiliana masuala mbalimbali ya kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Ethiopia.

Katika mazungumzo hayo, Balozi Kaganda aliishukuru Serikali ya Ethiopia kwa kuendelea kudumisha urafiki wa muda mrefu na Tanzania, huku akisisitiza kuwa uhusiano huo ulianzishwa na waasisi wa mataifa haya mawili, Hayati Baba wa Taifa wa Tanzania, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, pamoja na Hayati Mfalme Haile Selassie wa Ethiopia.

Balozi Kaganda ameipongeza Ethiopia kwa maandalizi ya uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwezi Juni 2026, akieleza kuwa Tanzania ni mshirika wa karibu wa Ethiopia, ambapo amewatakia wananchi wa nchi hiyo amani, umoja na mshikamano katika kipindi chote cha uchaguzi huo.

Kwa upande wake, Balozi Abdulwahid amemshukuru Balozi Kaganda kwa kutenga muda wake kwa ajili ya mazungumzo hayo huku akibainisha kuwa hatua hiyo si tu ishara ya uhusiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizi mbili, bali pia inaonesha namna Tanzania na Ethiopia zinavyoendelea kuthamini misingi ya kindugu iliyowekwa na waasisi wa mataifa hayo.

Vilevile, alieleza kuwa anatambua mchango unaotolewa na Tanzania kwa Ethiopia katika majukwaa ya kikanda na kimataifa, ikiwemo kuunga mkono jitihada za nchi hiyo katika kuwania nafasi mbalimbali katika taasisi na majukwaa hayo.

Katika hatua nyingine, Balozi Kaganda alitembelea Ubalozi wa Jamhuri ya Indonesia nchini Zimbabwe kwa ajili ya kutoa salamu za rambirambi kufuatia kifo cha aliyekuwa Makamu wa Rais Mstaafu wa Indonesia, Jenerali Mstaafu Try Sutrisno, aliyefariki dunia tarehe 02 Machi 2026.

Ziara hiyo ilikuwa ni ishara ya mshikamano na kuendeleza mahusiano mazuri ya kidiplomasia kati ya Tanzania na Indonesia.











Machi 5 2025, wanawake wa Chuo Kikuu Mzumbe wameadhimisha Siku ya Wanawake Duniani kwa kufanya matendo ya huruma kwa jamii inayowazunguka kwa kutembelea Kituo cha Afya Mlali kilichopo Wilaya ya Mvomero, mkoani Morogoro.

Ikiwa ni sehemu ya kusambaza upendo kwa jamii, wanawake wa Chuo Kikuu Mzumbe wamekabidhi msaada wa vifaa mbalimbali pamoja likiwemo tanki la maji lenye uwezo wa kuhifadhi lita 5,000 ili kusaidia upatikanaji wa maji safi na salama katika kituo hicho.

Mbali na tanki hilo, wanawake hao wametoa vifaa tiba, sabuni za maji, vifaa vya kuwekea uchafu (dustbins), vizolea uchafu, mifagio, pampers za watoto na vitambaa vya kufutia watoto (wipes) pamoja na vinywaji kwa wagonjwa. Wanawake hao wametoa vifaa hivyo kwa lengo la kuboresha mazingira ya utoaji huduma pamoja na kuwafariji wagonjwa katika kituo hicho.

Naye Naibu Makamu Mkuu wa Chuo – Taaluma, Utafiti na Ushauri, Prof. Hawa Tundui Petro, alisema Chuo kimekuwa kikiadhimisha siku hii kwa kufikia jamii zenye uhitaji.

“Kwa takribani miaka nane sasa, Chuo Kikuu Mzumbe kimekuwa kikiadhimisha siku hii, ikiwa ni sehemu ya kutekeleza kaulimbiu ya Chuo, “Tujifunze kwa Maendeleo ya Watu.”

Aliongeza kuwa kaulimbiu ya mwaka huu, “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi Kufikia Dira 2050,” inalenga kutambua mchango wa wanawake katika nyanja mbalimbali ikiwemo elimu, afya, siasa na uchumi.

Naibu Makamu Mkuu wa Chuo – Mipango, Fedha na Utawala, Prof. Allen Mushi, aliwataka wanawake kuendelea kushirikiana na kusaidiana katika jamii huku akisisitiza umuhimu wa usawa wa kijinsia.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Taasisi ya Taaluma za Maendeleo, Prof. Elizabeth Lulu Genda, alisema taasisi hiyo itaendelea kushirikiana na jamii katika kutatua changamoto mbalimbali na kuimarisha maisha ya wananchi.

Akizungumza kwa niaba ya kituo hicho, Kaimu Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Mlali, Dkt. Celestine Luzinga, aliwashukuru wanawake wa Chuo Kikuu Mzumbe kwa msaada wao, akisema vifaa hivyo pamoja na tanki la maji vitasaidia kwa kiasi kikubwa katika kuimarisha mazingira ya utoaji huduma kwa wagonjwa na kuongeza ufanisi kwa watumishi wa afya.

Baadhi ya akina mama waliopokea zawadi walisema: “Tunashukuru sana kwa msaada huu, hakika huu ni upendo na mmetutiq moyo sana.”

Ziara hii ni mfano wa jinsi wanawake wa Chuo Kikuu Mzumbe wanavyoshirikiana na jamii kuendeleza mshikamano, kusaidia wenye uhitaji, na kuimarisha usawa wa kijinsia katika jamii.

Vilevile, ziara inaashiriaa jinsi wanawake wa Chuo Kikuu Mzumbe wanavyoshirikiana na jamii kuendeleza mshikamano, upendo, kusaidia wenye uhitaji na kuimarisha usawa wa kijinsia katika jamii.





Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi akizungumza na ujumbe wa Kituo cha Umahiri wa Masuala ya Sayansi na Usimamizi Endelevu wa Ardhi kutoka Nchi za Kusini mwa Afrika (SASSCAL) wakati wa mazungumzo baina yao yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam Machi 06, 2026.

***************

Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi amekutana na kufanya mazungumzo na Ujumbe kutoka Kituo cha Umahiri wa Masuala ya Sayansi na Usimamizi Endelevu wa Ardhi kutoka Nchi za Kusini mwa Afrika (SASSCAL).

Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika Machi 06, 2026 Jijini Dar es Salaam, ujumbe huo ulifanya ziara kwa ajili ya kujitambulisha na kuwasilisha maombi ya ushirikiano baina yake na Serikali.

Kupitia mazungumzo hayo, Mwenyekiti wa Bodi ya Kituo hicho Prof. Gabriel Miguel alieleza masuala mbalimbali ikiwemo muundo na shughuli za kituo na miradi iliyotekelezwa katika nchi wanachama.

Kwa mujibu wa Prof. Miguel ameeleza utaratibu wa kujiunga na mtandao wa kituo hicho kwa nchi wanachama unaobainisha fursa na faida mbalimbali ikiwemo mapambano ya mabadiliko ya tabianchi, usimamizi endelevu wa ardhi na uhifadhi wa mazingira.

Aidha ameeleza kuwa taasisi hiyo imeendelea kujenga uwezo wa kitaalamu katika masuala ya kiufundi, ujenzi wa miundombonu na programu za masomo ya elimu ya juu kwa wataalamu katika nchi wanachama.

“Kituo kimefanya tafiti za masuala ya kilimo hifadhi, bayoanuai, mifumo ikolojia na nishati mbadala na kuhakikisha matokeo ya tafiti hizi yanaakisi mipango ya maendeleo katika nchi wanachama” amesema Prof. Miguel.

Prof. Miguel ameeleza kuwa kituo hicho kimekuwa kikifanya kazi kwa karibu na wadau mbalimbali wa maendeleo ikiwemo Serikali, mashirika ya mazingira, wadau wa viwanda na taasisi za kikanda.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi amekishukuru kituo hicho kwa kufanya ziara Tanzania na kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuhamasisha uhifadhi endelevu wa mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Aidha Dkt. Muyungi alieleza dhamira dhati ya Serikali kujiunga na kituo hicho ambapo aliainisha vipaumbele na maeneo ya ushirikiano ambayo ni muhimu kuzingatiwa kulingana na malengo ya kuanzishwa kwa taasisi hiyo.

“Tunashukuru kwa ziara hii ambayo imekusudia kuimarisha wigo wa ushirikiano katika nyanja ya sayansi, hili ni jambo muhimu kwa Serikali ya Tanzania hususani katika kipindi hiki tunachoelekea katika utekelezaji wa dira ya maendeleo ya taifa 2050” amesema Dkt. Muyungi.

Dkt. Muyungi pia alitoa ushauri kuhusu umuhimu wa kuundwa kwa timu ya pamoja ya wataalamu kati ya kituo na wataalamu watakaopendezwa na serikali ili kujadili kwa kina kuhusu faida zitakazopatikana iwapo Tanzania itaridhia kujiunga na taasisi hiyo.

SASSCAL ni kituo cha utafiti kuhusu masuala ya mabadiliko ya tabianchi, tathimini ya mazingira na usimamizi endelevu wa mazingira. Nchi wanachama wa Kituo hicho ni Angola, Botswana, Namibia na Afrika Kusini.
Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi akizungumza na ujumbe wa Kituo cha Umahiri wa Masuala ya Sayansi na Usimamizi Endelevu wa Ardhi kutoka Nchi za Kusini mwa Afrika (SASSCAL) wakati wa mazungumzo baina yao yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam Machi 06, 2026. Kushoto ni Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Mhe. Balozi Baraka Luvanda
Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi akizungumza na ujumbe wa Kituo cha Umahiri wa Masuala ya Sayansi na Usimamizi Endelevu wa Ardhi kutoka Nchi za Kusini mwa Afrika (SASSCAL) wakati wa mazungumzo baina yao yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam Machi 06, 2026. Kushoto ni Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Mhe. Balozi Baraka Luvanda na Mkurugenzi Msaidizi Mazingira Dkt. Kaninzio Manyika
Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi akizungumza na ujumbe wa Kituo cha Umahiri wa Masuala ya Sayansi na Usimamizi Endelevu wa Ardhi kutoka Nchi za Kusini mwa Afrika (SASSCAL) wakati wa mazungumzo baina yao yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam Machi 06, 2026. Kushoto ni Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Mhe. Balozi Baraka Luvanda na Mkurugenzi Msaidizi Mazingira Dkt. Kaninzio Manyika
Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo Kituo cha Umahiri wa Masuala ya Sayansi na Usimamizi Endelevu wa Ardhi kutoka Nchi za Kusini mwa Afrika (SASSCAL)Prof. Nelaga Indongo (katikati) akizungumza wakati wa kikao baina yao na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi kilichofanyika Jijini Dar es Salaam Machi 06, 2026. Kulia ni Kiongozi wa ujumbe huo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Kituo hicho, Prof. Gabriel Miguel.
Mwenyekiti wa Bodi ya Kituo cha Umahiri wa Masuala ya Sayansi na Usimamizi Endelevu wa Ardhi kutoka Nchi za Kusini mwa Afrika (SASSCAL) Prof. Gabriel Miguel akizungumza jambo wakati wa kikao baina yao na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi kilichofanyika Jijini Dar es Salaam Machi 06, 2026. Kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo hicho, Prof. Nelaga Indongo.
Mkurugenzi Msaidizi wa Mazingira Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Kaninzio Manyika akizungumza jambo wakati wa kikao baina yao na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi (kushoto) na Kituo cha Umahiri wa Masuala ya Sayansi na Usimamizi Endelevu wa Ardhi kutoka Nchi za Kusini mwa Afrika (SASSCAL) kilichofanyika Jijini Dar es Salaam Machi 06, 2026.
Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhe. Balozi Baraka Luvanda (katikati) akizungumza jambo wakati wa kikao baina yao na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi na Kituo cha Umahiri wa Masuala ya Sayansi na Usimamizi Endelevu wa Ardhi kutoka Nchi za Kusini mwa Afrika (SASSCAL) kilichofanyika Jijini Dar es Salaam Machi 06, 2026. Kuliani Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi.
Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi akipokea nakala ya taarifa kuhusu muundo na majukumu ya Kituo cha cha Umahiri wa Masuala ya Sayansi na Usimamizi Endelevu wa Ardhi kutoka Nchi za Kusini mwa Afrika (SASSCAL) kutoka kwa Mwenyekiti wa Bodi ya Kituo hicho Prof. Gabriel Miguel muda mfupi baada ya kumalizika kwa kikao baina yao kilichofanyika Jijini Dar es Salaam Machi 06, 2026.
Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi akipokea nakala ya taarifa kuhusu muundo na majukumu ya Kituo cha cha Umahiri wa Masuala ya Sayansi na Usimamizi Endelevu wa Ardhi kutoka Nchi za Kusini mwa Afrika (SASSCAL) kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo hicho Prof. Nelago Indongo muda mfupi baada ya kumalizika kwa kikao baina yao kilichofanyika Jijini Dar es Salaam Machi 06, 2026.
Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Ujumbe wa Kituo cha Umahiri wa Masuala ya Sayansi na Usimamizi Endelevu wa Ardhi kutoka Nchi za Kusini mwa Afrika (SASSCAL)uliongozwa na Mwenyekiti wa Bodi ya Kituo hicho Prof. Gabrel Miguel muda mfupi mara baada ya kumalizika kwa kikao baina yao Jijini Dar es Salaam Machi 06, 2026.

(PICHA NA OFISI YA MAKAMU WA RAIS)


Top News