Na Oscar Assenga, Tanga

Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Tanga kimeeleza kuwa suluhisho la kudumu la kuboresha eneo la kuchezea katika Uwanja wa CCM Mkwakwani ni uwekaji wa nyasi bandia, huku wakipanga kushirikiana na wadau wa soka kufanikisha mpango huo.

Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua uwanja huo, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga, Rajab Abdurahman, alisema uwekaji wa nyasi bandia unakadiriwa kugharimu kati ya shilingi milioni 400 hadi 500.

Ziara hiyo ni sehemu ya ukaguzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo mkoani humo, ikiwemo ile inayotekelezwa kwa fedha zinazotolewa na Serikali chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa lengo la kupunguza kero kwa wananchi.

Abdurahman aliwataka viongozi wa CCM, ambao ni wamiliki wa uwanja huo, kutumia ubunifu na kushirikiana na wadau wa soka ili kuhakikisha wanapata fedha za kuweka nyasi bandia.

“Tutawaomba wadau wa soka nchini watakapohitajika kutusaidia, kwani dhamira yetu ni njema. Kama ambavyo wamekuwa wakitusaidia hapo awali, tunaamini watashiriki nasi kuhakikisha tunakuwa na uwanja wa kisasa zaidi,” alisema.

Alieleza kuwa maboresho ya uwanja huo yatasaidia kuinua uchumi wa Mkoa wa Tanga, kwani utaweza kutumika kwa mashindano ya kitaifa na kimataifa, ikiwemo CECAFA na michuano mingine ya Afrika.

“Tunapokuwa na uwanja mzuri, hata timu za nje zitakuja kucheza hapa Tanga. Hii itaongeza mzunguko wa fedha na kukuza uchumi wa mkoa wetu,” aliongeza.

Aidha, alikumbusha kuwa uwanja huo uliwahi kufungiwa kutokana na kutokidhi vigezo, hasa ubora wa eneo la kuchezea, akisisitiza kuwa hatua zinazochukuliwa sasa zinalenga kuhakikisha viwango vinazingatiwa kwa usalama wa wachezaji na ubora wa mchezo.

“Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) linapofungia uwanja si kwa kupenda, bali kuhakikisha viwango vinazingatiwa. Ndiyo maana tumekuwa wepesi kuchukua hatua za maboresho,” alisema.

Katika hatua nyingine, Abdurahman alieleza kuridhishwa na maendeleo ya ufungaji wa viti 6,500 vilivyotolewa na TFF chini ya Rais wake, Wallace Karia, licha ya kuwepo kwa ucheleweshaji mwanzoni.

Amesema tayari ameagiza kazi hiyo ikamilike ndani ya mwezi mmoja, na kwa sasa inaendelea vizuri chini ya usimamizi wa Mjumbe wa Kamati ya Siasa ya Mkoa, Nasoro Makau.

Kwa mujibu wa mpango huo, maeneo ya kipaumbele ni jukwaa kuu pamoja na sehemu za mashabiki wa klabu za Coastal Union na African Sports. Pia wameomba viti vingine 2,500 ili kukamilisha uwanja mzima.

Abdurahman aliishukuru Serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, inayoongozwa na Waziri Paul Makonda na Naibu wake Hamisi Mwinjuma, pamoja na Rais wa TFF Wallace Karia, kwa ushirikiano wao katika kuboresha uwanja huo.

Alisisitiza kuwa maboresho hayo yanalenga kuhakikisha klabu za Coastal Union na African Sports zinaendelea kucheza mechi zao za nyumbani mkoani Tanga badala ya kuhamishiwa maeneo mengine.

Aidha, aliwataka mashabiki wa soka kujitokeza kwa wingi uwanjani kuunga mkono timu zao.

“Haileti maana kuwa na uwanja mzuri halafu mashabiki wanabaki nyumbani kuangalia mechi,” alisisitiza.

Kwa upande wake, Meneja wa Uwanja wa Mkwakwani, Nasoro Makau, alisema hadi sasa wamefikia asilimia 40 ya ufungaji wa viti na wana uhakika wa kukamilisha kazi hiyo ndani ya mwezi mmoja.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ametoa wito kwa vijana kusimama imara na kulinda umoja, kujenga uadilifu, kutumia elimu na ubunifu katika kukuza maendeleo ya nchi ili kuweza kumuenzi Baba wa Taifa Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere kwa vitendo.

Makamu wa Rais ametoa wito huo wakati akifungua Kongamano la Vijana katika Kumbukizi ya Miaka 104 ya Kuzaliwaa Baba wa Taifa, Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere, lililofanyika Ukumbi wa Chimwaga mkoani Dodoma, leo tarehe 11 Aprili 2026. Amesema ni muhimu kwa vijana kutambua wajibu wa msingi wa kizazi hiki, kwa kuhakakikisha wanafanya kila jitihada kuimarisha misingi ya kujitegemea kiuchumi, kiakili na kimaamuzi ili kuijenga nchi.

 Makamu wa Rais amesema Hayati Baba wa Taifa alikuwa kiongozi aliyeunganisha Taifa na kutoa mchango mkubwa katika ukombozi wa Bara la Afrika. Amesema Taifa la Tanzania lilipata bahati ya pekee kuwa na Hayati Mwl. Nyerere kwa kuwa alichukia rushwa, ubadhirifu na matumizi mabaya ya madaraka. Aliamini katika utu na uhuru wa mwanadamu ikiwemo msisitizo wa kuhakikisha kila wananchi anapata elimu.

Ameongeza kwamba Baba wa Taifa alitengeneza misingi ya amani, utulivu na mshikamano katika Taifa pamoja na kufundisha vitu vyote vinavyoweza kuleta mpasuko kama vile ukabila, dini, rangi, kupuuza maendeleo na usawa katika jamii.

Makamu wa Rais amesema ni dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kuendeleza mshikamano na umoja ambao Baba wa Taifa aliujenga.

 Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi wa Taasisi ya Kumbukumbu ya Mwal. Nyerere ambaye ni Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Mizengo Pinda ametoa rai kwa vijana kuhakikisha wanafanya jitihada za kujifunza historia ya Taifa ili kufahamu waliotoa mchango mkubwa katika historia hiyo.

Amewahimiza kusoma vitabu vilivyoandikwa kuhusu Hayati Mwal.Julius Kambarage Nyerere ili kufahamu mchango mkubwa aliyoutoa katika ukombozi wa Bara la Afrika na msisitizo alioutoa wa katika kuhakikisha umoja wa Afrika. Ameongeza Taasisi hiyo imejikita katika kutoa mchango kwa kuwasaidia viongozi vijana kuwa wazalendo na wanaowajibika.

 Kongamano hilo limejadili mada mbalimbali zenye lengo la kuwajengea vijana uzalendo, uwajibikaji, matumizi sahihi ya mitandao na matumizi bora ya fursa zilizopo nchini.






Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, tarehe 11 Aprili, 2026 akiwa Ikulu, Dodoma, amezungumza kwa njia ya mtandao na Chuo Kikuu cha Jimbo la Nasarawa, Keffi nchini Nigeria, kufuatia kutunukiwa Shahada ya Uzamivu ya Heshima kwa kutambua mchango wake katika maendeleo ya Bara la Afrika.

Katika hotuba yake, Rais Samia alieleza mshangao wake alipopokea taarifa ya tuzo hiyo kupitia barua kutoka kwa Mheshimiwa Abdullah Isule, Gavana wa Jimbo la Nasarawa. Alisema kilichomgusa zaidi ni kutambuliwa kwa mchango wake katika maendeleo ya Afrika, akibainisha kuwa anapokea heshima hiyo kwa unyenyekevu mkubwa na shukrani.

Amesisitiza kuwa tuzo hiyo si yake binafsi, bali ni ishara ya juhudi za pamoja za Watanzania na matarajio yao ya maendeleo, ushirikiano na ustawi wa binadamu.

Akielezea historia yake, Rais Samia alisema ametoka katika familia ya kawaida na kulelewa katika mazingira ya kijijini yaliyojengwa katika misingi ya unyenyekevu, bidii na maadili ya kijamii. Aliongeza kuwa elimu yake ya awali Zanzibar ilimfungulia macho kuhusu changamoto zinazowakabili wasichana wengi, ikiwemo ukosefu wa rasilimali na mitazamo hasi ya kijamii inayowazuia wanawake kushiriki kikamilifu katika maendeleo.

Amesema uzoefu huo ulimjengea azma ya kupambana na vikwazo hivyo si kwa manufaa yake binafsi pekee, bali kwa ajili ya wanawake na wasichana wengine.

Katika safari yake ya uongozi na utumishi wa umma, Rais Samia amejikita katika kuwawezesha wanawake na wasichana kwa kuhamasisha ushiriki wao katika uongozi, elimu na shughuli za kiuchumi. Alisisitiza kuwa hakuna jamii inayoweza kufikia maendeleo ya kweli ikiwa itawaacha nyuma wanawake, ambao ni sehemu kubwa ya jamii.

Aidha, Rais Samia amesema kuwa juhudi zake katika ustawi wa wanawake na watoto zimechangia kuteuliwa kwake na Umoja wa Afrika kuwa kinara wa afya ya mama na mtoto. Pia amewahi kuwa kinara wa biashara huru ya Afrika kwa wanawake na vijana, pamoja na kinara wa nishati safi ya kupikia barani Afrika.

Hotuba yake ilihitimishwa kwa kusisitiza umuhimu wa kuendeleza mshikamano na ushirikiano miongoni mwa mataifa ya Afrika ili kufanikisha maendeleo endelevu na ustawi wa watu wake.


Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma .

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ametoa wito kwa wanawake na vijana barani Afrika kuongeza juhudi, kujituma na kujiamini katika ndoto zao ili kufanikisha maendeleo ya binafsi na ya kijamii.

Rais Samia ametoa kauli hiyo leo Aprili 11, 2026, mara baada ya kutunukiwa shahada ya heshima na Chuo Kikuu cha Nasarawa, tukio ambalo limebeba heshima kubwa kwa uongozi wake na mchango wake katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Akizungumza baada ya tukio hilo, Rais Samia amesema safari yake ya uongozi ni ushahidi tosha kwamba mafanikio yanawezekana hata pale mtu anapokutana na changamoto mbalimbali za maisha, mradi tu awe na bidii, ujasiri na maono ya mbali.

Amebainisha kuwa Serikali na yeye binafsi wamekuwa mstari wa mbele katika kuhamasisha ushiriki wa wanawake katika nafasi za uongozi, elimu na sekta ya uchumi, akisisitiza kuwa hakuna jamii inayoweza kufikia maendeleo kamili iwapo nusu ya nguvu kazi (wanawake) haitashirikishwa kikamilifu.

Aidha, amewahimiza wahitimu kutumia elimu waliyoipata kama chachu ya mabadiliko chanya katika jamii zao, kwa kuanzisha miradi, kubuni suluhisho za changamoto za kijamii, na kuwa viongozi wenye maono.

Pia amesisitiza umuhimu wa kuzingatia maadili mema, uwajibikaji na uzalendo, akieleza kuwa mambo hayo ni msingi muhimu katika kujenga taifa imara na kuimarisha maendeleo ya Afrika kwa ujumla.

Hotuba yake imepokelewa kwa hisia chanya, ikichukuliwa kama ujumbe wa matumaini kwa kizazi cha vijana na wanawake wanaojitahidi kufikia mafanikio katika mazingira yenye changamoto mbalimbali.



SAME.

MAKAMU wa Rais na Waziri Mkuu mstaafu, John Samuel Malecela amesema kuwa, swala la Utalii kokote Duniani linaenda sambamba na swala la Amani na Utulivu na kuwaomba wananchi kuhakikisha wanalinda Amani ili kukuza Utalii nchi na kuendelea kujinufaisha kupitia sekta hiyo.

Malecela alitoa kauli hiyo jana wakati wa Uzinduzi wa tamasha la Same Utalii festival lililofanyika katika viwanja vya stendi wilayani Same mkoani Kilimanjaro ambapo alisema kuwa, utalii ni kite ambacho huchangia kuleta fedha za kigeni.

Alisema kuwa, baadhi ya nchi ulimwenguni serikali zinaendeshwa kwa fedha za Utalii na kuwataka kulichukulia swala hilo kwa umakini mkubwa.

Kiongozi huyo alidai kuwa, misingi ya Utalii ni ukarimu kwa wageni na kuwataka wananchi wa wilaya ya Same kuwa mfano katika ukarimu ili kukuza Utalii wa wilaya ya Same.

"Hata sehemu kukiwa na njiwa 10,000 wamejaa lakini jiwe likigonga tu wote wanakimbia kwa hiyo na sisi utalii wetu uanze na sisi wenyewe Watanzania kuwa na Amani ni jambo la msingi sana kwani Amani ndio italeta na kuwakaribisha watalii na ndio itatufanya tuendelee kukua kiuchumi" Alisema Malecela.

Na kuongeza "Swala la ukarimu kwa wageni ni kitu muhimu sana mahali pengine watu hawaendi kwa sababu hakuna moyo wa kuwapokea wageni lakini kwetu same tuwe na moyo wa kuwapokea wageni ili kukuza utalii wetu".

Alisema kuwa, kinachotuunga pamoja ni Amani na kuwasihi Watanzania kuendelea kuitunga na mambo mengine yatafuata.

"Ili Utalii wa same uweze kukua ni lazima uanze na sisi wenyewe wanasama kuwa na moyo dhabiti wa ukarimu ili wanapokuja na kurudi wakatoe sifa ni kweli wataenda kuona wanyama lakini mkiwakaribisha kwa moyo upande hawatarudi tena" Alisema Malecela.







Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo, amesema Tanzania inaendelea kujizatiti kusawazisha maendeleo ya kiuchumi, uendelevu wa mazingira, na usalama wa bahari.

Waziri Kombo amesema hayo alipozungumza katika Mkutano wa Tisa wa Bahari ya Hindi Aprili 10 2026, jijini Port Louis, Mauritius.

“Tanzania, kupitia juhudi za uhifadhi, ushirikishwaji wa jamii, na ushirikiano wa kikanda, inaendelea kulinda mifumo ya ikolojia ya bahari ya Hindi na kuimarisha usalama katika maji ya eneo lake, Ila mafanikio ya kudumu yatategemea ushirikiano imara zaidi kati ya nchi zinazopakana na bahari ya Hindi”, alisisitiza.

Balozi Kombo alihimiza nchi zinazopakana na bahari ya Hindi kuthibitisha wajibu wa pamoja na kushirikiana kuilinda bahari hiyo ili iendelee kuwa chanzo cha amani, ustawi, na fursa kwa vizazi vya sasa na vizazi vijavyo.

Alieleza kuwa Bahari ya Hindi ni nguzo muhimu ya ukuaji wa uchumi na ushirikiano wa kikanda kwa Tanzania, na ni lango muhimu linalounganisha nchi jirani zisizo na bandari na masoko ya dunia.

Aidha, alieleza kuwa kupitia uwekezaji wa kimkakati katika kuboresha na kuimarisha miundombinu ya bandari na nishati, Tanzania inaendelea kujiweka kama kitovu muhimu cha biashara, usafirishaji na huduma za baharini katika Afrika Mashariki na Kati na kwamba uchumi wa buluu unachangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya taifa, ukisaidia mamilioni ya watu na kukuza sekta za uvuvi, utalii, usafiri wa baharini na biashara za pwani.

Balozi Kombo alisema kaulimbiu ya mkutano huo ya “Uwajibikaji wa Pamoja kwa Usimamizi wa Bahari ya Hindi,” inaendana kikamilifu na hali halisi kwa sasa, na kwamba Bahari ya Hindi inakabiliwa na changamoto za mvutano wa kisiasa, vitisho vya usalama wa baharini vinavyoendelea kubadilika, pamoja na shinikizo la kimazingira.

“Changamoto hizi zinaonyesha umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya mataifa husika na kuwa uwajibikaji wa pamoja si hiari tena ni suala la lazima ili kuhakikisha kuwa bahari ya Hindi inakuwa salama, endelevu, na yenye manufaa kwa wote wanaoitegemea,” alisisitiza.













JESHI la Polisi Mkoa wa Rukwa linaendelea na mapambano dhidi ya wahalifu mbalimbali wakiwemo wale wanaosababisha taharuki katika jamii kwa kuzusha kuibiwa sehemu nyeti za miili yao na wale wanaowafanyia ukatili na udhalilishaji watoto.

Katika kuhakikisha jamii ya watu wa Mkoa wa Rukwa wanaishi bila hofu, limewafikisha mahakamani tena vijana watatu waliomzushia bwana Hosea Ngogo (31) mkazi wa Soweto Mbeya kuwaibia nyeti zao katika kijiji cha Kilangawana wilaya ya Sumbawanga kisha kumpiga na kumsababishia jeraha kichwani.

Vijana hao ambao ni Geofrey Milumba Deminic (24), Jafari Nebart Shanjila (25) wakazi wa Kijiji cha Kilangawana pamoja na Huruma Geofrey Kasonso (18) mkazi wa Kijiji cha Kilyamatundu, wametiwa hatiani na mahakama ya mwanzo Kipeta mbele ya Mhe. Hakimu Wilgis Mbunda.

Wote watatu wamepewa adhabu ya kifungo cha miezi sita jela kila mmoja, pia kumlipa fidia ya maumivu na jeraha alilopata bwana Hosea Amani Ngogo kiasi cha Tsh.50,000/= kila mmoja. Adhabu hiyo imetolewa 10 April, 2026 na hakimu huyo huku akisema iwe funzo kwa wote wanaozusha mambo ya kishirikina na kuleta hofu katika jamii ya watanzania waliostaarabika.

Kwa upande mwingine, mahakama ya wilaya ya Nkasi tarehe 09 Aprili 2026, imemhukumu Wandu Frolian Chimukole (30) mkazi wa kijiji cha Mbwendi wilayani Nkasi kutumikia kifungo cha miaka 30 jela baada ya kupatika na hatia ya kumbaka binti mwenye umri wa miaka 13. Mshitakiwa huyu alitenda kosa hilo tarehe 20 Januari 2026 huko kijiji cha Kakoma Wilaya ya Nkasi. Wakati akitoa adhabu hiyo Mhe. Hakimu Denis Luwungo alisema adhabu hiyo iwe onyo kwa wanaume wenye tabia ya kuwafanyia ukatili watoto wadogo.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Rukwa linatoa wito kwa wananchi wote kuendelea kutii sheria za nchi, pia wazazi kuendeleza ulinzi wa watoto ili wasifanyiwe ukatili.

Imetolewa na:
Kamanda wa Polisi,

Mkoa wa Rukwa.


Na Mwandishi Wetu

TANZANIA imeendelea kung’ara katika anga la kimataifa baada ya kuingiza vipengele 41 katika Tuzo za Utalii na Usafirishaji Duniani (World Travel Awards), hatua inayoimarisha nafasi yake kama moja ya vinara wa utalii barani Afrika.

Akizungumza, Aprili 11,2026 jijini Dar es Salaam, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano wa Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), Paulina Mkama, amesema tuzo hizo zinahusisha jumla ya washindani 85 kutoka sekta za umma na binafsi, zikilenga kutambua na kusherehekea ubora wa huduma, kuhamasisha ushindani na kutoa fursa kwa wadau na watalii kupigia kura vivutio bora duniani.

Paulina  ameeleza kuwa ushiriki wa Tanzania katika tuzo hizo ni fursa adhimu ya kuitangaza nchi kimataifa na kuiweka katika ramani ya dunia kama kitovu cha utalii. 

Ameongeza kuwa taasisi za serikali, ikiwemo TFS na TAWA, zimefanikiwa kuwasilisha vivutio vyake katika kinyang’anyiro hicho.

Kwenye kinyang’anyiro hicho , Tanzania imewania nafasi katika vipengele mbalimbali barani Afrika, huku vivutio vikubwa kama Hifadhi ya Taifa ya Serengeti vikitajwa kuwania tuzo za juu. Aidha, katika baadhi ya vipengele, washindani saba kati ya 14 wanatoka Tanzania, hali inayoonesha uimara na ushindani wa sekta ya utalii nchini.

Amebainisha kuwa sekta ya utalii inachangia zaidi ya ajira milioni moja kila mwaka, na mafanikio katika tuzo hizi yataongeza fursa za uwekezaji, ajira pamoja na kukuza pato la taifa.

Kwa sasa, kampeni ya “Kura Moja, Tiketi Moja kwa Tanzania” inaendelea, huku Watanzania na wadau wa utalii wakihamasishwa kushiriki kikamilifu kupigia kura nchi ili kuongeza nafasi ya ushindi.

“Mbali na kuimarisha ushindani wa ubora wa huduma, tuzo hizo pia huchochea ukuaji wa sekta ya utalii kupitia ubunifu, uwekezaji na kuongeza mvuto wa vivutio katika soko la kimataifa,” amesema Paulina.

Ameongeza kuwa  kwa mara ya kwanza, baadhi ya vivutio vinavyosimamiwa na taasisi za serikali kama TAWA na TFS ikiwemo Mpanga Kipengere, Aman Forest Reserve, Selous Game Reserve, Pugu Kazimzumbwi na Kilwa Kisiwani, vimeingia kwenye ushindani huo, jambo linaloashiria kukua kwa sekta ya utalii nchini.





Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi INEC ambaye pia ni Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume, Ndg. Ramadhani Kailima akizungumza katika kikao hicho cha Baraza.
Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu), Dkt. James Henry Kilabuko (wapili kulia) akishiriki kuimba Wimbo wa Wafanyakazi wakati wa ufunguzi wa Barala la Wafanyakazi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi lililokutana leo Aprili 11, 2026 mkoani Morogoro. Wengine pichani ni Mwenyekiti wa Baraza hilo na Mkurugenzi wa Uchaguzi wa INEC, Ramadhani Kailima (wapili kushoto), Katibu wa Baraza, Livini Avith (kulia) na Kulia ni mtumishi wa Tume, Rose Tengu.
Sehemu ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi la Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi wakishiriki kuimba Wimbo wa Wafanyakazi wakati wa ufunguzi wa Kikao cha Barala la Wafanyakazi INEC lililokutana leo Aprili 11, 2026 mkoani Morogoro.
Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu), Dkt. James Henry Kilabuko akizungumza wakati wa kufungua baraza la Wafanyakazi la INEC.

Na Mwandishi Wetu, Morogoro
WATUMISHI wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi wametakiwa kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia katiba, sheria, kanuni na taratibu na kuepuka lugha zozote za uchochezi zinazoweza kuleta uvunjifu wa amani na kuhatarisha maisha ya Watanzania.

Hayo yamesemwa leo Aprili 11, 2026 na Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu), Dkt. James Henry Kilabuko kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt Jimmy Yonaz wakati akifungua kikao cha Baraza la Wafanyakazi la Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, katika kikao kilichoketi Mkoani Morogoro.

“Napenda kuwaasa, kuzingatia katiba, sheria, kanuni na taratibu mnapotekeleza majukumu ya Tume na kuepuka lugha zozote za uchochezi zinazoweza kuleta uvunjifu wa amani na kuhatarisha maisha ya Watanzania,”alisema Dkt Kilabuko.

Dkt. Kilabuko amesema, taasisi ina malengo yake, upo uwezakano wa kuepusha migogoro ya ndani na nje ya taasisi inayoweza kuathiri utekelezaji wa majukumu ya Tume kwa ufanisi.

Mapema akimkaribisha Mgeni Rasmi, Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi INEC ambaye pia ni Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume, Ndg. Ramadhani Kailima alisema kwa sasa Tume inaendelea na zoezi la uandishi wa Taarifa ya Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani ya Mwaka 2025.

“Tume imekamilisha Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 ambao ulifanyika tarehe 29 Oktoba, 2025. Kwa sasa Tume inaendelea na zoezi la uandishi wa Taarifa ya Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani ya Mwaka 2025. Taarifa hiyo baada ya kukamilika, itawasilishwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,”alisema Kailima.

Aidha, amesema Tume ipo katika maandalizi ya uchaguzi mdogo wa Ubunge katika Jimbo la Isimani mkoani Iringa kufuatia kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Jimbo hilo, Mhe. William Lukuvi pamoja na uchaguzi wa udiwani katika Kata mbalimbali nchini ambazo madiwani wake walifariki.

Katika Kikao hicho cha siku moja pia kilitumika kwa kufanya uchaguzi wa Katibu wa Baraza hilo ambapo wajumbe walimchagua Ndg. Mwitaru Keboya kuwa Katibu mpya wa Baraza akichukua nafasi ya Ndg. Livini Avith ambaye amemaliza muda wake.
Katibu Mpya wa baraza la Wafanyakazi INEC, Ndg. Mwitaru Keboya akizungumza.

Katibu wa Baraza aliyemaliza muda wake, Ndg. Livini Avith akizungumza.


Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi INEC wakifuatilia agenda mbalimbali katika mkutano huo.


Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi INEC wakifuatilia agenda mbalimbali katika mkutano huo.

Mwenyekiti wa TUGHE tawi la INEC, Ndg. Juvenile Kaiza akizungumza.


Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi INEC wakifuatilia agenda mbalimbali katika mkutano huo.

Top News