-Magereza 12 Morogoro Yanufaika na Mradi wa Nishati Safi ya Kupikia kutoka REA     

Jeshi la Magereza Mkoa wa Morogoro limeendelea kuhamasishwa matumizi ya nishati safi ya kupikia ikiwa ni sehemu ya Mkakati wa Serikali kuhakikisha Asilimia 80 ya wanatumia wahamie kutumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.

Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua miradi ya nishati safi ya kupikia kwa Jeshi la Magereza mkoani Morogoro, Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Mhe. Balozi Meja Jenerali (Mstaafu), Jacob Kingu amesema kuwa lengo la taifa la kufikia matumizi makubwa ya nishati safi ya kupikia linawezekana kutokana na uwepo wa vyanzo mbalimbali vya nishati hiyo.

Amesema wananchi wana nafasi ya kuchagua aina ya nishati safi kulingana na mazingira wanayoishi, ikiwemo gesi, mkaa mbadala pamoja na matumizi ya umeme kwa ajili ya kupikia.

“Inawezekana ifikapo mwaka 2034 asilimia 80 ya watanzania wanatumia nishati safi za kupikia maana zipo nyingi" amesema Mwenyekiti Kingu.

Aidha, ameeleza kuwa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) unaendelea kupeleka huduma ya umeme katika Vijiji na Vitongoji jambo litakalowezesha wananchi wengi zaidi kutumia umeme kama chanzo cha nishati safi ya kupikia.

Kwa upande wake, Mkuu wa Magereza Mkoa wa Morogoro, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Magereza (SACP), Peter Anatory amesema mradi wa majiko ya nishati safi ya kupikia unaotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umewezesha magereza 12 ya Mkoa wa Morogoro kunufaika na huduma hiyo.

Amesema kupitia mradi huo, magereza hayo yamepata majiko 15 yanayotumia mkaa rafiki kwa mazingira pamoja na tani 236 za mkaa huo, hali iliyosaidia kuongeza matumizi ya nishati safi katika taasisi za magereza.

“Mradi huu umekuwa kichocheo kikubwa kwa magereza katika kuhakikisha tunatumia nishati safi ya kupikia,” amesema Anatory.

Naye Kamishna Msaidizi wa Magereza (ACP) Samuel Aron Mwakatika amesema matumizi ya nishati safi yana mchango mkubwa katika kuboresha maisha ya wananchi, kulinda mazingira pamoja na kukuza uchumi wa taifa.

Amesema katika Chuo cha Udereva KPF Kingolwira, matumizi ya nishati safi yamesaidia kuokoa muda uliokuwa unapotea kwa wanafunzi kwenda kutafuta kuni.

“Katika chuo hiki tuna wanafunzi 381, hivyo zamani ilikuwa lazima kuwe na kundi la wanafunzi wanaokwenda kutafuta kuni jambo lililokuwa linapunguza muda wa kujifunza. Nishati safi imesaidia kuondoa changamoto hiyo,” amesema Mwakatika.

Aidha, Mrakibu Mwandamizi wa Magereza (SSP), Nicostatus Magori amesema gereza hilo liliacha kutumia kuni kwa ajili ya kupikia chakula cha wafungwa tangu Desemba mwaka 2024 baada ya kuanza kutekelezwa kwa mradi huo wa kufungiwa mifumo ya nishati safi ya kupikia katika magereza. 







Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiagana na viongozi mbalimbali kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam kabla ya kuondoka nchini, kuelekea Kigali, Rwanda kushiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali kuhusu Uvumbuzi wa Nishati ya Nyuklia barani Afrika (NEISA) tarehe 19 Mei, 2026.

Mkutano huo wa Kimataifa unawakutanisha pia wataalamu wa nishati, wawekezaji na mashirika ya kimataifa, ambapo utajadili matumizi ya nishati ya nyuklia kwa maendeleo ya Bara la Afrika. Mkutano huo pia unalenga kujadili namna bora ya kuongeza upatikanaji wa nishati ya umeme Afrika, kupunguza uchafuzi wa mazingira, kusaidia maendeleo ya viwanda, kukuza ubunifu wa teknolojia za nishati ya nyuklia pamoja na kuvutia wawekezaji katika miradi ya nishati


 

Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela imefanya ziara katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa lengo la kujifunza namna ya utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya maendeleo ili kuboresha ukusanyaji wa mapato, kuinua uchumi na kuboresha upatikanaji wa huduma kwa jamii.

Ziara hiyo ilihusisha madiwani pamoja na wataalamu kutoka Manispaa ya Ilemela waliotembelea miradi mbalimbali kwa ajili ya kujifunza mbinu za usimamizi na utekelezaji.

Akizungumza kuhusu miradi hiyo, Mchumi katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Mataso Ndege, alisema kuwa lengo la utekelezaji wa miradi hiyo ni kuongeza mapato ya halmashauri, kupunguza utegemezi kwa serikali kuu, kuvutia uwekezaji, kupendezesha jiji pamoja na kuongeza ajira na huduma kwa wananchi.

“Utekelezaji wa miradi ya kimkakati umegawanyika katika awamu tatu ambapo awamu ya kwanza imehusisha ujenzi wa Government City Complex (Mtumba Complex), Dodoma City Hotel pamoja na Soko la wazi la Machinga, ambayo yote imekamilika. 

Awamu ya pili itahusisha miradi ya Nyerere Square Plaza na Nunge Investment Building, huku awamu ya tatu ikijumuisha Dodoma City Complex Mall, Dodoma City Complex Apartment na NK Complex” alisema Ndege.

Nae, Mtakwimu kutoka Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Nora Mulambo ya alisema kuwa mradi wa Dodoma City Hotel uligharimu shilingi bilioni 11.9, huku mradi wa Mtumba Complex unaojumuisha ukumbi wa mikutano unaotekelezwa kwa awamu tatu nao utagharimu jumla ya shilingi bilioni 59. 

Alifafanua kuwa awamu ya kwanza ya mradi huo iligharimu shilingi bilioni 18 na mradi umekamilika kwa asilimia 99. Aidha, alisema kuwa ujenzi wa Soko la wazi la Machinga uligharimu shilingi bilioni 9.5 na manufaa ya miradi hiyo yanaonekana kutokana na makusanyo ya mapato.

Kwa upande wake, Naibu Meya wa Manispaa ya Ilemela, Kuruthum Abdallah alisema kuwa ziara hiyo imelenga kupata uzoefu na mbinu zinazotumiwa na Halmashauri ya Jiji la Dodoma katika kusimamia miradi ya maendeleo.

 “Tumekuja kujifunza na kubadilishana uzoefu ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo na utoaji wa huduma bora kwa wananchi” alisema Abdallah.

Ziara hiyo inatarajiwa kuimarisha ushirikiano kati ya halmashauri hizo mbili pamoja na kuongeza uwezo wa kiutendaji katika kusimamia na kutekeleza miradi ya maendeleo yenye tija kwa wananchi.






 Dkt. Maghembe azindua Kongamano la Vijana wa Kitanzania chini ya Umoja wa Mataifa (TIMUN 2026) asisitiza umuhimu wa nafasi vijana katika kuleta Maendeleo Endelevu Kitaifa na Ulimwenguni

Leo tarehe 18 Mei 2026, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Ngwaru Jumanne Maghembe (Mb) amemwakilisha Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwenye uzinduzi wa Kongamano la Vijana wa Kitanzania chini ya Umoja wa Mataifa (Tanzania International Model United Nations -TIMUN 2026)  linalofanyika Zanzibar. Katika Hotuba yake, Mhe. Naibu Waziri Dkt. Maghembe amesisitiza umuhimu wa nafasi ya vijana katika kuleta maendeleo endelevu na mabadiliko chanya, kupitia teknolojia, diplomasia na ubunifu katika ngazi na Taifa na Ulimwenguni.

Mkutano wa TIMUN 2026, ni jukwaa muhimu la kimataifa linalolenga kukuza viongozi vijana, wanadiplomasia, wabunifu, na mawakala wa mabadiliko ambalo hufanyika kila mwaka chini ya uratibu wa Chama cha Vijana katika Umoja wa Mataifa Tanzania  (Youth of United Nations Association Tanzania-YUNA).

Mhe. Maghembe ameipongeza YUNA Tanzania kwa kuwawezesha vijana na kuendeleza maadili ya Umoja wa Mataifa miongoni mwa vijana wa Tanzania na Afrika kwa ujumla.

"Tumieni mkutano huu kubadilishana mawazo, kujenga ushirikiano, na kuibua suluhisho za changamoto mbalimbali zikiwemo mabadiliko ya tabianchi, ukosefu wa ajira, usawa wa kijinsia, na maendeleo ya teknolojia" alibaibisha Mhe. Maghembe












Na Mwandishi wa OMH

Dar es Salaam. Ofisi ya Msajili wa Hazina imekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa China nchini Tanzania, Chen Mingjian, pamoja na ujumbe wake, katika kikao kilicholenga kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi, uwekezaji na mageuzi ya mashirika ya umma.

Mazungumzo hayo yalifanyika jijini Dar es Salaam Jumatatu, Mei 18, 2026, kati ya menejimenti ya Ofisi ya Msajili wa Hazina ikiongozwa na Msajili wa Hazina, Nehemiah Mchechu, na ujumbe wa Ubalozi wa China ulioongozwa na Balozi wa China nchini Tanzania, Chen Mingjian.

Katika kikao hicho, pande hizo mbili zilijadili masuala ya uwekezaji wa serikali, usimamizi wa kampuni za umma na miradi ya kimkakati.

Akizungumza katika kikao hicho, Bw. Mchechu alisema Ofisi ya Msajili wa Hazina ina jukumu la kusimamia uwekezaji wa serikali katika taasisi na kampuni 308, ambapo 252 kati yake serikali ina hisa nyingi.

Alibainisha kuwa thamani ya uwekezaji wa serikali katika taasisi na kampuni hizo ni Sh92.3 trilioni.

Alisema uwekezaji huo unahusisha sekta mbalimbali zikiwemo usafiri wa anga, nishati, mafuta na gesi na madini, akisisitiza kuwa serikali inaendelea na mwelekeo wa kuongeza ufanisi na uhimilivu wa kifedha katika mashirika hayo.

Kwa upande wake, Balozi wa China nchini Tanzania, Chen Mingjian, alisema China itaendelea kuimarisha ushirikiano na Tanzania katika sekta za uwekezaji, miundombinu na mageuzi ya kiuchumi, akibainisha kuwa uhusiano wa nchi hizo mbili umejengwa katika msingi imara wa miaka mingi ya urafiki na imani ya kisiasa.

Balozi Chen aliongeza kuwa China itaendelea kusaidia jitihada za Tanzania katika kuendeleza viwanda, kuongeza thamani ya rasilimali za madini, pamoja na kuimarisha ushirikiano katika mafunzo na uhamishaji wa teknolojia kwa watumishi wa umma.

Aidha, alieleza kuwa China itaendelea kuunga mkono miradi ya kimkakati inayotekelezwa kwa ushirikiano kati ya nchi hizo mbili, ikiwemo sekta ya usafirishaji, nishati na uwekezaji wa pamoja katika kampuni za kimkakati.






Mwenyekiti wa UWT Taifa, Ndg. Mary Pius Chatanda (MCC), amewasha moto wa kampeni katika kata za Migoli na Kihorogota, kuelekea Uchaguzi Mdogo wa Jimbo la Ismani utakaofanyika tarehe 1 Juni, 2026.

Akizungumza na makundi mbalimbali ya wanawake na wananchi kwa ujumla, Ndg. Chatanda amebainisha kuwa CCM imeonyesha imani kubwa kwa kuweka mgombea mwanamke Ndg. Emmanuela Mtatifikolo Kaganda na sasa ni jukumu la wanawake wote kuungana na kushirikiana ili kupata ushindi.

Pia amepongeza ushirikiano mkubwa na uungwaji mkono kutoka kwa wanaume wa Ismani ambao wameonyesha nia ya dhati ya kumlinda na kumsaidia mgombea wetu ashinde.

Aidha, amewakumbusha kuwa Serikali imara ya awamu ya sita chini ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tayari ipo madarakani na inafanya kazi kubwa. Uchaguzi huu mdogo ni kwa ajili ya kupata mwakilishi bora atakayeenda kuendeleza mazungumzo ya kimaendeleo ya Ismani bungeni.















CHANGAMOTO ya afya ya akili imetajwa kuwa miongoni mwa matatizo makubwa yanayowakabili walinda amani wanaopelekwa katika misheni za kimataifa, wakiwemo kutoka Tanzania.

Mkuu wa Chuo cha Mafunzo ya Ulinzi wa Amani Tanzania (TPTC), Brigedia Jenerali George Itang’arealisema hayo jijini Dar es Salaam wakati wa ufunguzi rasmi wa programu mbili za kimataifa za mafunzo zilizolenga kuimarisha huduma za kitabibu na msaada wa kisaikolojia kwa walinda amani wanaofanya kazi katika mazingira yenye changamoto kubwa za kiusalama duniani.

Kozi hizo maalumu zinazojikita katika msaada wa kisaikolojia na uimarishaji wa uwezo wa kitabibu, zimewakutanisha wanajeshi, wataalamu wa afya na wakufunzi kutoka mataifa mbalimbali yakiwemo Canada, Rwanda, Cameroon, Indonesia, Urusi, Ujerumani na Marekani, hatua inayoonesha ushirikiano wa kimataifa katika juhudi hizo.

Brig. Gen. Itang’are alisema mtaala huo umeandaliwa mahsusi kuongeza uwezo wa walinda amani kutambua na kushughulikia changamoto kubwa za afya ya akili na matibabu wanazokutana nazo katika maeneo ya operesheni za mbele.

“Tumegundua kupitia uzoefu wa vikosi vya hivi karibuni kuwa kuna uhitaji mkubwa wa mafunzo ya aina hii kwa sababu walinda amani wanafanya kazi katika mazingira yenye msongo mkubwa unaoathiri afya ya akili na ustawi wa kijamii,” alisema.

“Ikiwa huna watumishi wenye afya njema, inakuwa vigumu kufikia ufanisi wa kiutendaji. Ndiyo maana mpango huu ni muhimu.”

Kamanda huyo alisema tathmini za hivi karibuni zilizofanywa katika operesheni za ulinzi wa amani zimebaini mapungufu makubwa katika huduma za msaada wa kisaikolojia na maandalizi ya kitabibu, hali iliyolazimisha kituo hicho kupanua kwa haraka programu zake maalumu za mafunzo.

Sehemu ya mafunzo ya kitabibu itatumia mfumo wa mafunzo kwa wakufunzi (training-of-trainers) ili kuimarisha mifumo ya afya kwa muda mrefu na kuongeza utayari wa kiutendaji kwa wanajeshi kabla na wakati wa misheni za kimataifa.

Wachambuzi walisema ushiriki wa wataalamu kutoka mataifa mbalimbali unaonesha kuongezeka kwa mwafaka wa kimataifa kuhusu umuhimu wa ushirikiano wa pande nyingi katika kulinda rasilimali watu inayobeba shughuli za ulinzi wa amani duniani.

Dkt. Annie Swai, mkufunzi mkuu wa afya ya akili na msaada wa kisaikolojia katika TPTC, alisema afya ya akili bado ni moja ya sekta zisizoeleweka vizuri katika huduma za afya licha ya athari zake kubwa katika mazingira ya kazi ya kijeshi.

Alionya kuwa matatizo ya kisaikolojia yasipotibiwa huendelea kuwa mabaya zaidi kadri muda unavyokwenda, hali inayopunguza uwezo wa utendaji kazi, kudhoofisha majukumu ya kijamii na kuyumbisha mshikamano wa taasisi.

Dkt. Swai alisema mazingira yenye presha kubwa katika misheni za ulinzi wa amani huwafanya wengi kubeba kimya kimya msongo mkali wa mawazo, wasiwasi na majeraha ya kihisia, hasa pale ambapo mifumo ya msaada wa taasisi haipo au haifikiki kwa urahisi.

"Changamoto za afya ya akili ni za kawaida na zinatibika, lakini watu wanahitaji mazingira salama ya kuzungumza waziwazi na kutafuta msaada bila hofu,” alisema.

Ili kushughulikia changamoto hizo kwa muda mrefu, Dkt. Swai alisema kituo hicho kinatarajia kuingiza rasmi mafunzo hayo katika mfumo wake wa kudumu wa mafunzo.

TPTC imejipanga kutoa mafunzo hayo angalau mara tatu kwa mwaka kwa lengo la kujenga uimara wa kisaikolojia kwa walinda amani kutoka mataifa yote yanayochangia vikosi vya ulinzi wa amani.







Jeshi Polisi mkoani Arusha limesema kwa kipindi cha kuanzia Aprili 18, 2026 hadi sasa, watuhumiwa 176 wamehukumiwa vifungo mbalimbali kwa makosa ulawiti, ubakaji, wizi, dawa za kulevya, kujeruhi, uvunjaji, kupatikana na nyara za serikali na kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu baada ya kufikishwa Mahakamani. 

Akitoa taarifa hiyo leo Mei 18, 2026 Kamanda wa Polisi Mkoani humo, SACP Justine Masejo amesema kati ya waliohukumiwa kwa makosa makubwa, mtuhumiwa 01 alihukumiwa kunyongwa hadi kufa kwa kosa la mauaji huku mtuhumiwa 01 akihukumiwa kifungo cha maisha gerezani kwa kosa la kulawiti, 

Ameendelea kufafanua kuwa watuhumiwa 02 walihukumiwa miaka 30 gerezani kwa makosa ya kubaka na wizi na watuhumiwa wengine 02 walihukumiwa miaka 20 gerezani kwa makosa ya unyang’anyi wa kutumia silaha na kupatikana na nyara za serikali.

Aidha, amebainisha kuwa kupitia operesheni dhidi ya dawa za kulevya, walifanikiwa kukamata watuhumiwa 19 wakiwa na Mirungi Kilogramu 90 na watuhumiwa 12 wakiwa na bhangi misokoto 177.

Pia kwa kipindi hicho walifanikiwa kukamata Watuhumiwa 33 wakiwa na Pombe ya moshi lita 434 na mitambo 09 ya kutengeneza pombe hiyo.

SACP Masejo amesema operesheni hizo zinaendelea kufanyika maeneo yote katika mkoa huo, ambapo amewataka baadhi ya watu wachache wanaojihusisha na vitendo vya kihalifu kuacha mara moja vitendo hivyo kwani watawakamata na kuchukua hatua za kisheria dhidi yao.

Sambamba na hilo, wataendelea kuchukua hatua kwa madereva wachache wanaoendesha vyombo vya moto kwa kutofuata sheria za usalama barabarani hususani mwendokasi, ulevi na kupita magari mengine bila kuchukua tahadhari.

Jeshi la Polisi mkoani humo limewapongeza wananchi wote wanaotoa taarifa za uhalifu na wahalifu katika maeneo yao hususani katika kipindi hiki kuelekea msimu mkubwa wa utalii katika Mkoa huo.



Na Anne Robi, Mtwara.

WANAFUNZI wa Majukwaa ya sekta ya mafuta na Gas (Oil and Gas Clubs) Mkoani Mtwara wameliomba Shirika la Maendeleo ya Petroli nchini  (TPDC) kuwaandalia ziara ya kutembelea miradi ya gesi asili kujifunza  kwa kuona namna gesi asilia inavyotumika kwenye magari na viwandani.

Wanafunzi hao wametoa wito huo leo tarehe 18 Mei, 2026 wakati wa mkutano wao na  shirika la TPDC waliotembelea majukwaa hayo kukagua maendeleo.

Mwanafunzi  kutoka shule ya sekondari Magamba Loveness Japhet amesema kupitia majukwaa shuleni wanapata elimu kuhusu masuala mbalimbali ya gesi asilia huku akiomba wanafunzi kuwezeshwa kufika kwenye miradi ya utekelezaji wa shughuli za TPDC kujifunza zaidi.

Mwalimu Mlezi wa Jukwaa la wanafunzi sekta ya mafuta na Gesi, shule ya Sekondari ya Wasichana Mkoani Mtwara, Aurelia Kimaro amesema wanafunzi wengi wanashauku ya kutaka kujua namna ambavyo gesi asilia inatumika kwenye magari na viwandani kuzalisha bidhaa mbalimbali.

"Wengi tunavyojua masuala ya gesi asilia ni mapana sana, kuna uchimbaji, utachakataji na pia utumiaji, tunaliomba Shirika la TPDC kuwaandalia wanafunzi ziara kwenye miradi ya utumiaji gesi hiyo kama viwandani na kwenye magari ili wanafunzi wajionee na kujifunza," amesema.

Afisa Maendeleo ya Jamii Mwandamizi  TPDC, Ali Muluge  amesema wanawawezesha wanafunzi ambao wanajiunga na majukwaa ya Mafuta na Gesi kupata elimu kwa kuwapa mahitaji ya kujifunzia na kuwawezesha kufika kwenye miradi mbalimbali ya uchimbaji, na utachakataji.

"Tumepokea ombi la wanafunzi hao kutaka sasa kufika kwenye miradi ambayo inajihusisha na utumiaji wa gesi kama vile viwandani, na tutalifanyia kazi, " amesema.

Amesema TPDC ilianzisha majukwaa ya mafuta na Gesi kwenye shule za sekondari 16 Mikoani Mtwara kwa lengo la kutoa taarifa na elimu sahihi kwa wanafunzi na walimu kuhusu shughuli za serikali kwenye sekta ya mafuta na Gesi.

"Lango lingine la kuanzisha majukwaa haya (Oil and Gas Clubs) ni kuchochea ari ya wanafunzi kupenda kusoma masomo ya Sayansi na kupata wataalamu ambao watalisaidia taifa kutekeleza shughuli kwenye sekta ya mafuta gesi," amesema.












Top News