Mbunge wa Jimbo la Kilombero, Abubakari Asenga, ametoa pole kwa wananchi wa jimbo hilo waliokumbwa na mafuriko makubwa yaliyosababishwa na mvua zinazoendelea kunyesha katika maeneo mbalimbali ya Halmashauri ya Mji wa Ifakara, mkoani Morogoro.

Akizungumza leo Machi 27, 2026 katika Ofisi ya Waziri Mkuu inayoshughulikia maafa, Mara baada ya kupokea msaada wa magodoro, mablanketi na chakula, Asenga amesema kuwa juhudi zinaendelea kuhakikisha wananchi waliopata madhara wanapata msaada wa haraka ili kupunguza athari walizokumbana nazo.

Mbunge huyo ameeleza shukrani zake kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, pamoja na Waziri Mkuu, Mwigulu Nchemba, kwa kuwezesha upatikanaji wa vifaa vya dharura kwa ajili ya kuwasaidia waathirika.

Amesema kuwa tayari wamepokea msaada unaojumuisha magodoro 75, mablanketi pamoja na tani 10 za mahindi, ambavyo vitasambazwa kwa wananchi waliokumbwa na mafuriko hayo wakati wakisubiri hatua zaidi za msaada kutoka serikalini.

Aidha, Asenga amewapongeza wananchi pamoja na kamati ya maafa ya wilaya kwa kushirikiana na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kwa juhudi kubwa walizozifanya kuokoa maisha ya watu. Amebainisha kuwa hadi sasa hakuna taarifa yoyote ya vifo iliyothibitishwa licha ya uharibifu mkubwa wa makazi ya wananchi.

Ameongeza kuwa baada ya kupokea taarifa za kuwepo kwa wananchi wasio na mahali pa kulala, ofisi yake ilichukua hatua za haraka kutafuta msaada wa magodoro, mablanketi pamoja na chakula ili kuhakikisha mahitaji muhimu yanapatikana kwa wakati.

Kwa upande mwingine, amesema ofisi ya mbunge imefanikiwa pia kupata unga ambao unatarajiwa kusambazwa kesho Jumamosi katika maeneo yaliyoathirika zaidi ikiwemo Ifakara, Lumemo na Michenga, ili kuwafariji na kuwasaidia wananchi waliokumbwa na adha hiyo.

Asenga amesisitiza kuwa wataendelea kuisimamia serikali kuhakikisha inatekeleza mipango ya kudhibiti athari za mafuriko, ikiwemo kufufua mabwawa, kupanua mito pamoja na kujenga miundombinu ya kinga kama matuta ili kupunguza madhara ya mafuriko siku zijazo.

Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa, takribani kaya 100 zenye jumla ya watu wapatao 500 zimeathirika na mafuriko hayo. Ingawa baadhi ya maeneo yameanza kupungua maji na wananchi kurejea makwao, bado wapo ambao hawajaweza kurudi kutokana na kiwango kikubwa cha maji kilichoingia kwenye makazi yao.

Kwa ujumla, juhudi za serikali zinaendelea kusaidia waathirika wa mafuriko katika Jimbo la Kilombero, huku msisitizo ukiwa ni kuhakikisha misaada ya dharura inawafikia wananchi wote walioathirika na kuweka mikakati madhubuti ya kudhibiti majanga kama haya siku zijazo.




NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) kwa kushirikiana na Tume ya Ushindani (FCC) wamekutana na wadau wa bidhaa za pombe nchini kwa lengo la kuwajengea uelewa juu ya matakwa ya sheria, kanuni na viwango vinavyosimamia sekta hiyo.

Kikao hicho kilichofanyika leo Machi 27, 2026 jijini Dar es Salaam, pia kimelenga kujadiliana na kubaini changamoto zinazowakabili wadau katika kukidhi matakwa ya kisheria pamoja na masuala ya ushindani, ili kupata ufumbuzi wake.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao hicho, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TBS, Mhandisi Yona Afrika, amesema kumekuwa na malalamiko yanayopokelewa na taasisi hizo kuhusu uwepo wa pombe duni na bandia katika soko, hali inayochangiwa na baadhi ya wafanyabiashara wasio waaminifu.

“Bidhaa hizi zisipozingatia matakwa yaliyowekwa, zinaweza kuhatarisha afya na usalama wa walaji,” amesema Afrika.

Ameongeza kuwa TBS kwa kushirikiana na FCC zitaendelea kuimarisha usimamizi wa viwango ili kudhibiti ubora wa bidhaa pamoja na kuhakikisha ushindani wa haki katika soko.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi.Roberta Feruzi, amesema uwepo wa pombe duni na bandia si tu unaharibu ushindani wa haki bali pia husababisha malalamiko kutoka kwa walaji kuhusu thamani ya fedha wanazolipa na athari za kiafya.

Amebainisha kuwa hali hiyo pia hudhoofisha biashara halali na kuvuruga mazingira ya ushindani sawa kwa wafanyabiashara wanaofuata sheria.








Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Wilaya ya Chamwino Mkoani Dodoma, limepanda zaidi ya miche ya miti elfu mbili ya vivuli pamoja na miche 420 ya matunda katika eneo lenye ukubwa wa heka tisa, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuunga mkono kampeni ya uhifadhi wa mazingira na kupambana na mabadiliko ya tabianchi.

Akizungumza Machi 27, 2026 wakati wa zoezi la upandaji miti,  lililofanyika katika eneo la ofisi za TANESCO wilayani humo, Mkuu wa Wilaya ya Chamwino, Mhe. Janeth Mayanja, amelipongeza shirika hilo kwa kuwa mstari wa mbele katika kuhamasisha upandaji miti kupitia kauli mbiu ya “Nitunze Nikutunze”.

Amesema wilaya hiyo imejiwekea lengo la kupanda miti laki mbili  katika kipindi hiki cha masika, ambapo miche tayari ipo katika vitalu vya Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Wilayani humo.

Aidha, amesema katika vijiji vyote 107 vya wilaya hiyo, miche ya miti elfu moja imegawiwa kwa kila kijiji na wananchi wamepewa bure ili kuipanda katika makazi yao na mashamba, hatua inayolenga kuongeza uoto wa asili na kuboresha mazingira.

Mhe. Mayanja ameongeza kuwa ndani ya miaka mitatu, eneo hilo linatarajiwa kuwa na miti mingi itakayosaidia kutoa kivuli, matunda pamoja na hewa safi kwa wananchi wanaofika kupata huduma mbalimbali kwenye ofisi hiyo.

Kwa upande wake, Meneja wa TANESCO Wilaya ya Chamwino, Mhandisi Judith Beatus, amesema zoezi hilo ni utekelezaji wa agizo la Rais Samia Suluhu Hassan la kuhimiza wananchi kushiriki kikamilifu katika utunzaji wa mazingira.

Naye mwakilishi wa Meneja wa TANESCO Mkoa wa Dodoma, James Vesso, amesema lengo la kupanda miti hiyo ni kuboresha mandhari ya Jiji la Dodoma na kuongeza kuwa shirika hilo limejipanga kuhakikisha miti yote iliyopandwa inalindwa na kukua vizuri.

Kipekee amemshukuru Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Lazaro Twange, kuwezesha zoezi hilo kwa kutenga rasilimali fedha, huku akisisitiza kuwa juhudi za upandaji miti zitaendelea kuwa endelevu ndani ya shirika hilo.

Kwa ujumla, juhudi hizi zinaonesha dhamira ya dhati ya TANESCO na Serikali katika kulinda mazingira, huku wananchi wakihimizwa kuendelea kushiriki kikamilifu katika upandaji na utunzaji wa miti kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.







 

 

Zaidi ya wanafunzi 400 wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi wamenufaika na huduma za bure za uchunguzi wa afya katika kambi maalum iliyoandaliwa na Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi Hesabu Tanzania (NBAA) kwa kushirikiana na Unique Group, ikiwa ni sehemu ya kurudisha kwa jamii katika maadhimisho ya miaka 30 ya kampuni hiyo.

Akizungumza wakati wa tukio hilo lililofanyika jijini Dar es Salaam siku ya Ijumaa, Mwenyekiti wa Bodi ya NBAA, CPA Prof. Sylivia Temu, alisema mpango huo unaonesha ushirikiano imara kati ya taasisi hizo mbili na kusisitiza umuhimu wa kuweka kipaumbele cha afya kwa vijana wanaojiandaa kufanya mitihani ya kitaaluma.

“Hatua hii inathibitisha ushirikiano wetu mzuri na Unique Group, kampuni inayotoa huduma za ukaguzi na uhasibu. Katika kuadhimisha miaka 30 tangu kuanzishwa kwake, wameamua kusherehekea kwa kuandaa kambi ya matibabu kwa gharama zao wenyewe kwa kushirikiana na Aga Khan Hospital,” alisema Temu.

Temu alibainisha kuwa lengo la kambi hiyo ni kutoa huduma za kinga kwa wanafunzi wanaojiandaa kufanya mitihani ya Bodi, akisisitiza kuwa afya njema ni msingi muhimu wa mafanikio ya kitaaluma na tija ya muda mrefu.

Alieleza kuwa uchunguzi huo unahusisha magonjwa mbalimbali ikiwemo matatizo ya macho, kisukari, saratani ya mlango wa kizazi pamoja na magonjwa ya zinaa. Aidha, waandaaji wameahidi kusaidia matibabu kwa hadi vijana 50 watakaobainika kuwa na changamoto za kiafya wakati wa zoezi hilo.

“Lengo kuu ni kuwakumbusha vijana kuwa afya yao ni muhimu katika kufanikisha malengo yao ya kitaaluma. Pia tumekuwa tukiwafikia kupitia majukwaa ya kidijitali, jambo linaloeleza mwitikio mkubwa tunaouona leo,” aliongeza, huku akiwahimiza vijana wengi zaidi kujiunga na taaluma ya uhasibu ambayo inalenga kulinda maslahi ya umma.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Unique Group, CPA Dr. B. S. Sree Kumar, alisema kambi hiyo ni sehemu ya uwajibikaji wa kampuni kwa jamii (CSR) katika kuadhimisha miaka 30 ya utoaji huduma.

“Tunapoadhimisha miaka 30, hii ni njia yetu ya kushukuru jamii. Tunarejesha kwa kushirikiana na NBAA, huku timu ya madaktari kutoka Aga Khan Hospital wakitoa huduma za uchunguzi wa afya ikiwemo sukari, macho, moyo, saratani ya matiti na matatizo mengine,” alisema Kumar.

Dk. Kumar alisisitiza kuwa kampuni hiyo iko tayari kusaidia wanafunzi watakaogundulika na matatizo ya afya wakati wa uchunguzi, akibainisha kuwa taasisi zinapaswa kurudisha kwa jamii kutokana na mchango wanaoupata.

Naye mwanafunzi wa CPA, Catherine Madembwe, alisema mpango huo umekuja kwa wakati muafaka na una manufaa makubwa, akibainisha kuwa vijana wengi hawana utaratibu wa kupima afya zao mara kwa mara.

“Tukio hili ni muhimu kwa sababu linatupa fursa ya kupima afya zetu ambayo mara nyingi hatupati. Nashauri kampuni nyingine ziige mfano huu kwa kuwa watu wengi hawana utamaduni wa kujichunguza afya zao, jambo linaloeleza mwitikio mkubwa unaoonekana,” alisema Madembwe.
Mwenyekiti wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) CPA Prof. Sylvia Temu akizungumza wakati wa ufunguzi wa huduma za bure za uchunguzi wa afya katika kambi maalum kwa wanafunzi wa mitihani ya uhasibu iliyoandaliwa na Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi Hesabu Tanzania (NBAA) kwa kushirikiana na Unique Group.
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania(​NBAA), CPA Pius A. Maneno akizungumza wakati wa ufunguzi wa huduma za bure za uchunguzi wa afya katika kambi maalum.
Mkurugenzi Mtendaji wa Unique Group, CPA Dr. B. S. Sree Kumar akizungumza kuhusu namna kampuni hiyo ilivyoweza kurudisha kwa jamii kwa kutoa huduma za bure za uchunguzi wa afya kwa wanafunzi wa wanaotegemea kufanya mitihani ya Bodi.
Wajumbe wa Bodi, watumishi wa NBAA pamoja na wanafunzi wa Mitihani ya Bodi wakifuatilia hotuba ya mgeni rasmi wakati wa ufunguzi wa huduma za bure za uchunguzi wa afya katika kambi maalum.
Huduma za uchunguzi wa afya ukiendelea

Na Mwandishi Wetu

Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo  na Mitaji (UN CDF) limesema kuwa linaendelea kuunga mkono juhudi za Serikali za kuhakikisha zaidi ya asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2030 kwa kusapoti matumizi ya nishati hiyo mashuleni na katika taasisi mbalimbali za umma hapa nchini.

Akiongea wakati wa kukabidhi majiko ya nishati safi ya kisasa  katika shule ya Msingi Bunge jijini Dar es Salaamz Peter Malika, Mshauri Mkuu wa Kiufundi wa UNCDF, amesema kupitia CookFund jumla ya shilingi bilioni 26 zimetolewa kama mikopo kwa biashara ndogo na za kati (SMEs) 102 zinazojihusisha na biashara ya nishati safi ya kupikia katika wilaya 14 za Dar es Salaam, Pwani, Morogoro, Dodoma na Mwanza.

Bw.Malika amesema pia kuwa wanafunzi 62,000 katika shule mbalimbali nchini Tanzania wamenufaika na mpango huo, huku UNCDF ikilenga kufikia taasisi 147 za umma ifikapo Septemba mwaka huu.

" Malengo yetu ni kuunga mkono ajenda ya nishati safi inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha asilimia zaidi ya 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi hapa nchini,"

" Tukiwa kama wadau, tunachukua hatua mbalimbali, ikiwemo kusaidia upatikanaji wa miundombinu katika shule mbalimbali hapa nchini na kuwa na program mbalimbali na wadau katika kuhakikisha kunakuwa na mazingira wezeshi ikiwemo sera za kuvutiwa wawekezaji katika sekta hii," amesema.

Ameongeza  kuwa UNCDF  wataendelea kutoa ushirikiano na wadau mbalimbali ikiwemo Serikali katika kuhakikisha nishati safi inafikiwa.

Amesema nishati safi ya kupikia inalinda mazingira na afya pamoja na kuokoa gharama inayotokana madhara ya matumizi ya mkaa na kuni.


Akiongea wakati wa kupokea msaada huo, Mwalimu Mkuu wa Shule ya Bunge Leonida Mlekule ameishukuru UNCDF kwa msaada huo wa kuhamaisha matumizi ya nishati safi na kuunba mkono mpango wa matumizi ya nishati safi hapa nchini.

Amesema kuwa majiko waliyoyapata kutoka UNCDF watayatunza ili kuendelea kupunguza gharama ya manunuzi.

Amesema matumizi ya mkaka yalikuwa yanaigharimu shule hiyo  zaidi ya milioni mbili, lakini kutokana na majiko hayo wameweza  kuokoa kiasi cha shilingi milioni moja na kuzipeleka katika matumizi mengine.

Mgeni rasmi katika makabidhiano hayo ya majiko ya kisasa alikuwa Naibu Waziri wa Nishati , Salome Makamba ambaye ameishukuru UNCDF kwa msaada huo na kuahidi ushirikiano zaidi katika kufanikisha ajenda hiyo ya matumizi ya nishati safi hapa  nchini.

" Tunaomba wadau wengine wajitokeze katika kusaidia mpango huu hapa nchini," amesema.

Mradi huo wa  kusambaza nishati safi ya kupikia katika Taasisi za Umma na Sekta Binafsi unafadhiliwa na Umoja wa Ulaya (EU).


Naibu Waziri amesema kuwa Taasisi za Umma na Sekta Binafsi zinazolisha watu zaidi ya  250 zinatakiwa kuwa na majiko ya kisasa yenye matumizi ya niashati mbadala ya kupikia katika kulinda afya na mazingira.

Amemtaja Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kuwa ni kinara wa nishati safi ya kupikia na kutoa wito wa kujitokeza na kumuunga mkono.


Amesema utekelezaji waje unawahusu wadau wote ikiwemo Taasisi za Umma ,  Sekta Binafsi  na wadau wa maendeleo hapa nchini,.

Naibu Waziri wa Nishati Salome Makamba akizungumza wakati wa Makabidhiano ya Nishati ya Safi ya Kupikia kwa Shule ya Msingi Bunge zilitolewa na UN CDF jijini Dar es Salaam.
Mshauri Mkuu wa Kiufundi wa UNCDF Peter Malika akizungumza kuhusiana na mikakati ya kusambaza nishati safi ya kupikia wakati hafla ya kukabidhi majiko ya kisasa ya kupikia katika shule ya Msingi Bunge jijini Dar es Salaam.
Naibu Waziri wa Nishati Salome Makamba akipata maelezo kutoka kwa Mwalimu Mkuu wa Shule Msingi Bunge Leonida Mlekule  kuhusiana na majiko yalitolewa na UNCDF kwenye shule ya Msingi Bunge jijini Dar es Salaam.
Picha ya pamoja ya meza kuu na wanafunzi wa Shule ya Msingi Bunge mara baada ya kukabidhiana majiko ya kissa katika Shule hiyo .


 

Na Munir Shemweta, WANMM


Watumishi wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Makao Makuu wamepatiwa mafunzo maalum ya lishe pamoja na mwongozo wa kudhibiti VVU/ UKIMWI na magonjwa yasiyoambukizwa, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuwaimarisha kiafya na kuongeza ufanisi wao kazini.

Mafunzo hayo ya siku moja yamefanyika tarehe 27 Machi, 2026 katika ofisi za wizara zilizopo Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma, yakilenga kuwajengea watumishi uelewa mpana kuhusu namna bora ya kujikinga na magonjwa pamoja na kuzingatia lishe bora katika maisha ya kila siku.

Akifungua mafunzo hayo, Kaimu Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa wizara hiyo, Bw. Deodatus Mwiliko, alisema kuwa afya ya mtumishi ni nyenzo muhimu katika kuongeza tija na ufanisi kazini, hivyo ni muhimu kwa watumishi kupewa elimu sahihi ya afya mara kwa mara.

Alieleza kuwa, Wizara ya Ardhu, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imejipanga kuhakikisha watumishi wake wanapata mafunzo mbalimbali yanayogusa ustawi wao, ikiwemo masuala ya afya, ili kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi.

Katika mafunzo hayo, mada kuhusu mwongozo wa kudhibiti VVU/UKIMWI na magonjwa yasiyoambukizwa iliwasilishwa na Bi. Juliana Ntukey kutoka Ofisi ya Rais – Utumishi, ambaye alisisitiza umuhimu wa kuzingatia miongozo iliyopo ili kulinda afya za watumishi na jamii kwa ujumla.

Aidha, mada ya lishe bora iliwasilishwa na Bi. Semeni Eva Juma, Afisa Lishe kutoka Jiji la Dodoma, ambapo alitoa elimu juu ya umuhimu wa kula mlo kamili na wenye virutubisho vinavyohitajika kwa afya bora ya mwili.

Kwa ujumla, mafunzo hayo yamepokelewa kwa hamasa kubwa na watumishi, huku yakitarajiwa kuwa chachu ya mabadiliko chanya katika kuimarisha afya na ustawi wao mahali pa kazi.
Bi. Juliana Ntukey kutoka Ofisi ya Rais – Utumishi akitoa mafunzo kuhusu muongozo wa kudhibiti VVU/Ukimwi na magonjwa sugu zyasiyoambukizwa kwa watumishi wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi jijini Dodoma tarehe 27 Machi 2026.







Sehemu ya watumishi wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi wakiwa katika mafunzo maalum ya lishe pamoja na mwongozo wa kudhibiti VVU/UKIMWI na magonjwa yasiyoambukizwa yaliyofanyika jijini Dodoma tarehe 27 Machi, 2026.
Bi. Juliana Ntukey kutoka Ofisi ya Rais – Utumishi akitoa mafunzo kuhusu muongozo wa kudhibiti VVU/Ukimwi na magonjwa sugu zyasiyoambukizwa kwa watumishi wa Wizara ya Ardhi Jijini Dodoma tarehe 27 Machi 2026.

Bi. Semeni Eva Juma, Afisa Lishe kutoka Jiji la Dodoma, akitoa elimu juu ya umuhimu wa kula mlo kamili na wenye virutubisho vinavyohitajika kwa afya bora ya mwili kwa watumishi wa wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi jijini Dodoma tarehe 27 Machi, 2026.






Baadhi ya watumishi wa Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi wakiwa katika mafunzo maalum ya lishe pamoja na mwongozo wa kudhibiti VVU/UKIMWI mahala pa kazi tarehe 27 Machi 2026 (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)








Top News