
Akifunga mafunzo hayo amewasisitiza viongozi hao wa elimu kwenda kuweka mkazo kwenye uongozi bunifu wa kimkakati unaoleta mabadiliko kama msingi wa maendeleo katika taasisi za elimu.
Pia amesisitiza juu ya uongozi jumuishi ambapo wanapaswa kushirikisha wadau, kusikiliza maoni ya jamii na kujenga mazingira ya uaminifu na uwajibikaji wa pamoja katika kufikia mafanikio ya usimamizi wa taasisi za elimu wanazozisimamia.
“Nawasihi mwende kuwa viongozi wenye maono, wenye uwezo wa kufanya maamuzi ya kimkakati, na ujuzi wa kusimamia mabadiliko ya taasisi mnazosimamia kwa ufanisi kwani ninyi ndio mtachochea mabadiliko hayo”. Ameeleza Dkt. Maulid.
Aidha, Makamu Mkuu wa Chuo Taaluma, Tafiti na Ushauri Elekezi Dkt. Lucas Mzelela amesema, mafunzo ya ADEM yamelenga kuwawezesha viongozi wa elimu kwa ujuzi wa vitendo, fikra za kimkakati na uwezo wa kusimamia taasisi za elimu kwa ufanisi ili kuleta mabadiliko ya kweli katika sekta ya elimu.
Nae Mwenyekiti wa TAHOSSA Mkoa wa Arusha, Mwalimu Omari Nyangu ameipongeza ADEM kwa namna ilivyoendesha mafunzo hayo kwa umahiri na weledi mkubwa na kutanabaisha kuwa maendeleo ya sekta ya elimu hayawezi kupatikana bila uwekezaji katika kuwajengea uwezo viongozi na wasimamizi wa taasisi za elimu na mafunzo waliyopatiwa ni dira katika usimamizi wa taasisi za elimu wanazozisimamia.
Wakuu hao wa shule wamejengewa uwezo kuhusu utawala bora wa elimu, Mpango wa Jumla wa Maendeleo ya Shule, usimamizi wa utekelezaji wa Mtaala, ustawi na usalama wa wanafunzi shuleni, ushirikishwaji wa jamii katika kuleta maendeleo ya shule, usimamizi wa rasilimali za shule, kuzingatia itifaki na huduma kwa wateja pamoja na ufuatiliaji na tathmini wa shughuli za elimu shuleni.






















-Aahidi Ushirikiano wa Kisheria katika Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira Nchini*
Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeungana na wadau wa mazingira katika hafla ya futari iliyoandaliwa kwa lengo la kuimarisha ushirikiano na kuendeleza mahusiano mazuri baina ya taasisi hiyo na wadau wake.
Hafla hiyo imefanyika Leo 26, 2026 katika Hoteli ya Serena, jijini Dar es Salaam, ambapo viongozi, watumishi wa Serikali na wadau binafsi walihudhuria tukio hilo lenye taswira ya umoja na mshikamano.
Akiongea katika hafla hiyo, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Bw. Hamza S. Johari aliipongeza NEMC kwa kuandaa tukio hilo lenye kujenga umoja na kukuza mshikamano miongoni mwa Taasisi za Serikali na wadau wa mazingira. Aidha, aliahidi kuendelea kutoa ushirikiano wa kisheria ili kuhakikisha Sheria na Kanuni za mazingira zinatekelezwa ipasavyo kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware Semesi, alipozungumza alisema futari hiyo ni sehemu ya utamaduni wa Baraza katika kujenga uhusiano wa karibu na wadau wake.
Alisisitiza umuhimu wa kudumisha maadili ya utu, heshima na ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu ya hifadhi ya mazingira nchini, akibainisha kuwa kupitia ushirikiano huo malengo ya kulinda na kuboresha mazingira yanaweza kufikiwa kwa ufanisi zaidi.
Katika hatua nyingine Katibu Tawala wa Mkoa wa Dar es Salaam, Ndg. Abdul Rajabu Mhinte, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya NEMC na Ofisi ya Mkoa katika kusimamia na kutekeleza Sheria za mazingira. Aliahidi kuwa Ofisi ya Mkoa itaendelea kuunga mkono juhudi za uhifadhi na usimamizi endelevu wa mazingira kwa ustawi wa taifa.
Hafla hiyo imehudhuriwa pia na wadau wa mazingira wakiwemo JMAT, Bodi ya NEMC, watumishi wa Baraza, wawakilishi kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais pamoja na Taasisi za kibenki
ALN Tanzania, kampuni inayojishughulisha katika huduma za kisheria na ushauri wa biashara, imezitaka biashara za kifamilia nchini kuondokana na mifumo isiyo rasmi iliyowasaidia katika hatua za awali za ukuaji, na badala yake kukumbatia mifumo thabiti ya utawala bora.
Hatua hiyo itawezesha kulinda utajiri wa vizazi, kuhakikisha ustawi wa muda mrefu na kuvutia uwekezaji kutoka nje.
Wito huo ulitolewa wakati wa hitimisho la mfululizo wa semina za mafundisho ya kusimamia biashara za kifamilia katika mfumo sahihi ( Family Business Resilience & Growth Knowledge Series), zilizoandaliwa na ALN Tanzania kwa ushirikiano na International Finance Corporation (IFC) jijini Dar es Salaam wiki hii. Mfululizo huo semina hizo tatu ulijadili misingi ya utawala wa kifamilia, muundo wa bodi na katiba za familia katika awamu zilizopita, huku kikao cha mwisho kikijikita katika urithishaji na mpito wa uongozi.
Akizungumza katika semina hiyo, Shemane Amin, Mshirika wa ALN hapa nchini , alisisitiza kuwa mwendelezo wa biashara za kifamilia hauji kwa mazoea bali unapaswa kupangwa kwa makusudi.
“Biashara nyingi za kifamilia hukua kwa mafanikio katika miaka ya mwanzo kwa kutegemea imani na maamuzi yasiyo rasmi,” alisema. “Hata hivyo, kadri biashara zinavyopanuka na vizazi vinavyoongezeka kushiriki, kuweka mifumo rasmi kunakuwa muhimu kulinda biashara yenyewe na umoja wa familia.”
Alieleza kuwa kampuni hiyo ilianzisha mfululizo huo wa semina ili kuwapatia wamiliki wa biashara za kifamilia mifumo ya vitendo kuhusu utawala bora, upangaji wa urithishaji na uwazi wa uongozi mambo ambayo mara nyingi huamua iwapo biashara itaendelea baada ya kizazi cha mwanzilishi wa biashara (Founder) katika familia husika.
Kwa upande wake, Edward Williams, Mkurugenzi wa ALN Tanzania, alisisitiza umuhimu wa kuanza mapema kupanga urithishaji na kuonya dhidi ya mabadiliko ya uongozi yanayofanyika kwa dharura.
“Moja ya dhana potofu iliyoenea katika biashara za kifamilia ni kwamba urithishaji huanza pale mwanzilishi anapokuwa tayari kustaafu,” alisema. “Kwa uhalisia, urithishaji huanza mapema zaidi.
Mabadiliko yenye mafanikio ni yale ambayo ukuzaji wa uongozi, miundo ya wanahisa na mifumo ya utawala inakuwa tayari imewekwa tangu awali.”, alisema.
Alibainisha kuwa kadri biashara za Kitanzania zinavyokua kwa thamani na kuwa tata zaidi, mikataba rasmi ya wanahisa, katiba za familia, majukumu yaliyoainishwa wazi kwa watendaji wakuu na mifumo huru ya usimamizi vinakuwa muhimu katika kulinda thamani ya muda mrefu.
Naye Mona Doshi, Mshirika wa ALN kutoka Mombasa nchini Kenya, alizungumzia umuhimu wa sera rasmi za ajira kwa wanafamilia katika kuimarisha uimara wa biashara.
“Kadri familia zinavyopanuka kizazi hadi kizazi, kuwa na mwongozo wa uwazi kuhusu vigezo vya kuajiriwa, viwango vya utendaji na uwajibikaji husaidia kuzuia migogoro ya ndani na kuimarisha uongozi unaozingatia sifa,” alieleza.
Aliwahimiza wamiliki wa biashara kuweka mifumo rasmi ya utawala inayolinda urithi wa familia huku ikizingatia weledi, ili kuhakikisha mabadiliko ya uongozi yanategemea maandalizi na uwezo wa mtu badala ya kuchaguliwa kuongoza tu kwa sababu ni sehemu ya familia.
Akizungumza kwa niaba ya IFC, Rose Lumumba alisisitiza kuwa utawala bora uliowekwa kwa mifumo rasmi unahusishwa moja kwa moja na utayari wa kupokea uwekezaji na ustawi wa muda mrefu.
“Biashara za kifamilia zinazoweka mifumo ya utawala mapema huwa katika nafasi nzuri zaidi ya kuvutia mitaji, kupanuka kwa uwajibikaji na kustahimili mabadiliko ya vizazi,” alisema.
Washiriki walikubaliana kuwa biashara za kifamilia zina mchango mkubwa katika uchumi wa Tanzania, na kwamba uwezo wake wa kuweka mifumo rasmi ya uongozi na utawala utaathiri uimara wa sekta binafsi kwa ujumla.
Tafiti za kimataifa zinaonesha kuwa ingawa biashara za kifamilia zinachangia zaidi ya asilimia 60 ya shughuli za sekta binafsi duniani, ni takriban asilimia 30 tu zinazofanikiwa kuvuka hadi kizazi cha pili, na chini ya asilimia 15 hufikia kizazi cha tatu. Wataalamu wa sekta hiyo wanaeleza kuwa upangaji madhubuti wa urithishaji na nidhamu ya utawala bora huongeza kwa kiasi kikubwa uwezekano wa mafanikio ya mpito huo.
ALN Tanzania hutoa ushauri kwa biashara za kifamilia kuhusu uundaji wa mifumo ya utawala, mipango ya urithishaji, makubaliano ya wanahisa na suluhisho za usimamizi wa utajiri wa kuvuka mipaka, ikiwawezesha kubadilika kutoka biashara zinazoongozwa na waanzilishi hadi taasisi imara za kudumu.

📍Yataja utendaji wake kama kiungo muhimu kwenye chama na serikali
*NA MWANDISHI WETU, MBEYA
Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Mbeya Vijijini, imemtunukia Tuzo maalum ya Heshima na Shukrani Mkuu wa Wilaya hiyo, Mhe. Solomon Itunda, kwa kutambua mchango wake mkubwa wa kuunganisha Serikali na Chama katika utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2020-2025.
Tuzo hiyo imekabidhiwa jana tarehe 26 Februari 2026, wakati wa kikao cha Halmashauri Kuu ya Wilaya kilichopokea na kujadili taarifa ya utekelezaji wa Ilani kwa kipindi cha mwezi Julai hadi Desemba 2025.
Akisoma maelekezo ya Kamati ya Siasa mbele ya wajumbe wa Halmashauri Kuu, Mwenyekiti wa CCM Wilaya Hakimu Mwalupimbi, amemuelezea DC Itunda kama "Kiungo" madhubuti ambaye amekuwa akipatikana wakati wote kushughulikia kero za wananchi na mahitaji ya Chama bila kujali muda.
"DC Itunda umekuwa kiungo kikubwa baina ya Chama na Serikali. Iwe usiku wa manene, asubuhi au mchana, umekuwa ukipokea simu na pale unapokuwa na majukumu mengine unajibu kwa ujumbe mfupi na baadaye unapiga simu kufuatilia. Hiyo ni ishara ya kiongozi aliyelelewa na kukomaa ndani ya Chama," alisema Mwenyekiti huyo.
Mwenyekiti aliongeza kuwa uzoefu wa DC Itunda uliotukuka—kuanzia nafasi ya Katibu wa CCM Mkoa wa Mbeya hadi ngazi ya Taifa—umechangia kwa kiasi kikubwa utulivu na mafanikio yanayoonekana sasa wilayani humo.
Alisisitiza kuwa tuzo hiyo ni ishara ya upendo na shukrani kutoka kwa wana-CCM ili kumtia moyo aendelee kukibeba Chama, hususan katika nyakati hizi za kuelekea majukumu mazito ya kitaifa.
Akizungumza kwa unyenyekevu baada ya kupokea tuzo hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Mhe. Solomon Itunda, amekishukuru Chama Cha Mapinduzi kwa malezi yaliyomfikisha katika nafasi hiyo ya utumishi wa umma.
Kamati ya Siasa ya Wilaya imebainisha kuwa utaratibu huo wa kutambua na kupongeza watendaji wanaofanya vizuri utakuwa endelevu ili kuongeza ari ya utumishi ndani ya Wilaya ya Mbeya.



.jpeg)





.jpeg)





















