Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete akiongoza Mkutano huo wa Bodi ya GPE.
Mwenyekiti wa Bodi ya Taasisi ya GPE Dkt. Jakaya Kikwete akiwa na viongozi wa Taasisi hiyo wakati wa Mkutano huo wa Bodi. Wa kwanza kushoto ni Bw. Charles North, Naibu Afisa Mtendaji Mkuu wa GPE anayetokea Marekani, Bi. Christine Hogan, Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya GPE anayetokea Canada, na kulia kwake ni Bi. Laura Frigenti, Afisa Mtendaji Mkuu anayetokea Italia.

RAIS Mstaafu Jakaya Dkt. Mrisho Kikwete, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Taasisi ya Kimataifa inayoshughulikia Masuala ya Elimu Duniani (Global Partnership for Education - GPE) ameendelea kuwa kinara katika kuhamasisha jitihada za upatikanaji wa fedha za kugharamia elimu kwa watoto wanaoishi katika mazingira magumu duniani.

Kwa nafasi yake ya Mwenyekiti wa Bodi ya GPE ameongoza Mkutano muhimu wa Bodi hiyo uliofanyika Paris, Ufaransa tarehe 3 - 4 Juni, 2025 ambao pamoja na mambo mengine umejadili mkakati wa GPE kukusanya kiasi cha Dola za Marekani bilioni 15 hadi kufikia mwaka 2030 chini ya Kampeni ijulikanayo kama GPE 2030. Mkutano huo wa Bodi ulihudhuriwa pia na Bi. Éléonore Caroit, Waziri wa Nchi wa Ufaransa anayeshughulikia masuala ya Ubia wa Kimataifa na Maslahi ya Wafaransa waishio Ng'ambo.

Kupitia ubia na ushirikiano kati ya Taasisi ya GPE, nchi wafadhili, mashirika ya kimataifa ya misaada, GPE imelenga kuwarejesha watoto takriban milioni 270 ambao hawapo mashuleni kote duniani, hususan kutokana na sababu mbalimbali. Aidha, fedha zinazokusanywa na GPE hutumika pia kugharamia uboreshaji wa elimu ya awali na ya msingi kwa watoto wanaoishi katika nchi za kipato cha chini na zinazoendelea, hususan watoto wa kike na wale wanaojikuta kwenye mazingira magumu kama vile ya vita, ukame, mafuriko, nk.

Kupitia Kampeni hiyo ya GPE 2030, jumla ya wanafunzi milioni 750 kutoka katika nchi 96 kote duniani watanufaika kupitia uboreshwaji wa mifumo ya elimu, ununuzi wa vitabu vya ziada na kiada, ujenzi na uboreshwaji wa madarasa, maabara, na mafunzo kwa walimu na kuwaongezea ujuzi.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Taasisi ya GPE baada ya Mkutano huo wa Bodi, nchi za Italia na Nigeria ndiyo zitaongoza Kampeni ya kukusanya fedha hizo katika hafla maalumu itakayofanyika tarehe 23 Septemba, 2026 pembezoni mwa Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UNGA).

Vilevile, taarifa hiyo imeeleza kuwa licha ya mabadiliko ya sasa ya hali ya kifedha duniani ambapo wafadhili mbalimbali, hususan nchi zilizoendelea, zinabadilisha vipaumbele vyao vya maeneo ya kuelekeza ufadhili, Taasisi ya GPE imeridhishwa na mwitikio mzuri wa nchi wafadhili kama vile Ujerumani, Australia, Ufaransa, nk ambazo tayari zimetangaza michango yao kwa kampeni hiyo. Aidha, taarifa hiyo imeeleza kuwa ni matarajio ya GPE elimu ya msingi itaendelea kuwa kipaumbele katika kipindi hiki cha mpito, huku Taasisi hiyo ikiahidi kuwa Taasisi ya mfano wa kuigwa wa ubia na ushirikiano wa kimataifa kwa kuzileta nchi pamoja kupitia lengo la kuboresha elimu ya msingi duniani.

Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa, Said Yakubu alihudhuria katika hafla iliyoandaliwa baada ya Mkutano huo. Ikumbukwe kuwa Tanzania ni moja ya nchi wanufaika wa fedha zinazotolewa na Taasisi ya GPE ambapo hadi sasa imeshapokea zaidi ya Dola za Marekani milioni 207.3 kwa ajili ya kuboresha sekta ya elimu nchini. Aidha, GPE imetenga takriban Dola za Marekani milioni 50 kwa ajili ya Tanzania ikiwa ni mwendelezo wa kuboresha sekta hiyo muhimu.



Na.Sophia kingimali.
WITO umetolewa kwa wanahabari Nchini kuendelea kufanya uchunguzi wa kina kuhusu masuala yanayohusu maendeleo ya bara la Afrika na kuhakikisha simulizi za Waafrika zinasimuliwa na Waafrika wenyewe.

Wito huo umetolewa Juni 4,2026 Jijini Dar es salaam na Mwandishi wa habari za uchunguzi na mtayarishaji wa filamu ya maandishi (documentary), David Hundeyin amesema Waafrika wanapaswa kuelewa kwa undani sababu zinazochangia matukio ya kisiasa yanayotokea barani humo badala ya kuamini kuwa yanachochewa na sababu za ndani pekee.

Amesema kuwa baadhi ya vyombo vikubwa vya habari vya kimataifa vinaendeshwa kwa kuzingatia maslahi ya nchi vinakotoka na hivyo huwasilisha habari kwa mtazamo unaoendana na malengo ya kisiasa ya mataifa hayo.

“Waandishi wa habari wanapaswa kutambua kuwa kila chombo cha habari kina mtazamo fulani. Ni muhimu kwa Waafrika kujenga uwezo wa kusimulia hadithi zao wenyewe na kuchambua taarifa wanazopokea kutoka vyanzo mbalimbali,” amesema.

Kwa upande wake Mwanazuoni na mchambuzi wa maswala ya maendeleo kutoka Zimbabwe Joshua Maponga Amesema kuwa bara la Afrika linapaswa kuwa makini na migogoro ya kijiografia na kisiasa kati ya mataifa makubwa duniani, akidai kuwa ushindani huo unaweza kuathiri mwenendo wa siasa na maendeleo katika nchi mbalimbali za Afrika.

Aidha, Maponga ametaka uchunguzi zaidi ufanyike kuhusu vyanzo vya fedha vinavyotumika na baadhi ya mashirika yasiyo ya kiserikali (NGOs), akisisitiza umuhimu wa uwazi na uwajibikaji katika matumizi ya fedha hizo.

Amesema serikali zinapaswa kuhakikisha mashirika yote yanayofanya kazi katika nchi zao yanaeleza kwa uwazi vyanzo vya mapato yao na namna fedha hizo zinavyotumika ili kuondoa mashaka yoyote kuhusu shughuli zao.

Hata hivyo, alisisitiza kuwa hoja zake hazilengi kuhalalisha vitendo vyovyote vinavyoweza kukiuka haki za wananchi, bali kuchochea mjadala kuhusu ushawishi wa maslahi ya nje katika masuala ya kisiasa na kijamii ya Afrika.

Na. Calvin Katera - Babati.

Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) imekutana na wadau wa utalii na uhifadhi ili kusuka mikakati itakayochagiza ongezeko la watalii na kuridhika kwa wageni watakaotembelea Hifadhi ya Taifa Tarangire. Mikakati hiyo imefanyika leo Juni 03, 2026 katika kikao cha pamoja kilichofanyika katika hifadhi hiyo inayosifika kwa tembo wengi na wakubwa nchini Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla. 

Kikao hicho ni hatua ya maandalizi kuelekea msimu mpya wa utalii (High season) unaoanza mwezi Juni hadi mwishoni mwa mwezi Januari kila mwaka. 

Katika kikao hicho Mkuu wa Kanda ya Kaskazini, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi Dkt. Beatrice Kessy alieleza kuwa wadau na wawekezaji kwa kushirikiana na hifadhi wanapaswa kutoa huduma bora zitakazoongeza hamasa na kuridhika kwa wageni ili waende kuisemea vizuri hifadhi na Taifa kwa ujumla. Kama inavyojulikana katika soko la utalii mgeni anaporidhika kwa huduma na mapokezi mazuri anaporudi nchini kwake huwa ni balozi mzuri kwa yale mema aliyofanyiwa. 

Sambamba na hilo Kamanda Kessy aliongeza; “Hifadhi ya Taifa Tarangire imeboresha miundo mbinu ya barabara na malazi. Aidha, ikolojia imeendelea kuimarishwa ili wanyamapori wapate malisho ya kutosha na wanyama waonekane kwa urahisi, kwani malisho yanapokuwa mengi wanyamapori hawatembei umbali mrefu hivyo kuwawezesha watalii kuona wanyama wote waliowakusudia katika safari yao

Kwa upande wake, Bw. Loseku Dorop kutoka Kampuni ya Conserve Safari alieleza kuwa wadau wa utalii wawekeze nguvu katika matumizi ya nishati safi, vitambulisho kwa watoa huduma wa makampuni ya kitalii na usafi wa mazingira kwa kuepuka kurusha taka, kwani taka huathiri mazingira na wanyamapori.

Kwa upande wake Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Tarangire Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi Dkt. Tutindaga George alieleza kuwa licha ya hifadhi hiyo kushika nafasi ya tatu kwa mapato na wingi wa watalii, mikakati yao ni kuwa ya pili au ya kwanza kuzipiku Hifadhi za Taifa Serengeti na Kilimanjaro.

Kikao hicho mbali na kuweka mikakati kuelekea msimu mpya wa utalii pia ni utaratibu wa hifadhi hiyo kukumbushana kanuni na taratibu mbalimbali za uhifadhi na kuwahamasisha wadau hao kuendesha utalii endelelevu kwa maslahi yao binafsi na maslahi ya Taifa kwa ujumla.





 







Rais Samia Suluhu Hassan amesema Shahada ya Uzamivu ya Heshima (Honoris Causa) aliyotunukiwa na Chuo Kikuu cha Urafiki wa Watu wa Urusi- (RUDN University) nchini Urusi, maarufu kama Patrice Lumumba University ni heshima kubwa kwake binafsi na kwa taifa la Tanzania kwa ujumla.

Akihutubia baada ya kutunukiwa shahada hiyo Rais Samia amesema katika dunia ya sasa inayobadilika kwa kasi kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia, ni muhimu kwa nchi kuwekeza katika wataalamu waliobobea ambao wanaelewa kuwa ujuzi wao ni chachu ya maendeleo endelevu ya taifa.

Ameongeza kuwa Tanzania itaendelea kuimarisha ushirikiano wa kimataifa katika sekta ya elimu, utafiti na teknolojia ili kuhakikisha vijana wanapata maarifa yatakayowezesha kushindana katika soko la ajira la kimataifa na kuchangia maendeleo ya kiuchumi.

Rais Samia ametunukiwa Shahada ya Uzamivu ya Heshima na Chuo Kikuu cha RUDN, kwa kutambua mchango wake katika uongozi bora, diplomasia na maendeleo ya jamii.

Shahada hiyo imetolewa wakati wa ziara ya kitaifa ya Rais Samia nchini Urusi, ambapo amekuwa akifanya mazungumzo ya kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi kati ya Tanzania na Urusi.
Na. Mwandishi wetu, DODOMA

VIONGOZI wa Serikali za Mitaa Halmashauri ya Jiji la Dodoma watakiwa kusimamia misingi ya maadili na mawasiliano ili kulinda imani ya wananchi katika huduma wanazopewa.

Rai hiyo imetolewa wakati wa mafunzo maalumu ya uongozi yaliyofanyika katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, yakilenga kuwajengea uwezo viongozi hao katika kusimamia rasilimali na kuhudumia umma kwa uadilifu, huku wakionywa kuwa mmomonyoko wa maadili duniani sasa ni tishio linalohitaji udhibiti wa pamoja.

Akiwasilisha mada kuhusu maadili na umuhimu wa mawasiliano katika uongozi, Mhadhiri kutoka Chuo cha Serikali za Mitaa (Hombolo), Ng'omange Merkiad alisisitiza kuwa kuwepo kwa taratibu na kanuni madhubuti za kimaadili ni jambo la lazima ili kuwepo na tabia inayofanana na inayotabirika wakati wa kuwahudumia wananchi. 

"Maadili sio masimulizi tu ya maneno, bali ni maelekezo ya vitendo yanayomwongoza kiongozi kujua nini cha kufanya na kwa wakati gani katika utekelezaji wa majukumu yake ya kila siku ya kiutawala" alisema Merkiad.

Akizungumzia dhamana ya uongozi, aliwakumbusha viongozi hao wa mitaa kuwa nafasi walizonazo ni matokeo ya imani kubwa ambayo serikali imewekeza kwao, hivyo wanapaswa kuilinda imani hiyo kwa wivu mkubwa kwa kuishi maisha ya uadilifu. 

"Imethibitika bila shaka yoyote kwamba uadilifu ni nyenzo kuu inayomwezesha kiongozi kuishi katika usafi wa kiutendaji, jambo ambalo ni msingi mkuu wa kujenga na kuimarisha imani ya wananchi kuelekea kwa viongozi wao wa ngazi za chini. Tusichoke kuwa waadilifu kwasababu tutaokoa kizazi kijacho" alisema Merkiad.

Nae, Katibu wa Vijana Platform Halamshauri ya Jiji la Dodoma, Jamal Mshumbusi aliyehudhuria mafunzo hayo alipongeza na kubainisha kuwa yatasaidia kwa kiasi kikubwa kuongeza ufanisi, uwajibikaji, na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi katika maeneo yao.

Usimamizi thabiti wa maadili na matumizi ya mawasiliano ya uwazi, viongozi hao sasa wanatarajiwa kuacha alama chanya na kuimarisha utawala bora, hatua itakayochochea maendeleo ya haraka na endelevu kuanzia ngazi ya mitaa hadi taifa kwa ujumla.



Na Jordan Mbwambo WF, Dodoma


Serikali imesema inaendelea kukamilisha mchakato wa uandaaji wa Kanuni za Bima za Kilimo ambazo zitasaidia kuongeza upatikanaji wa kinga kwa wakulima dhidi ya majanga yanayoathiri mazao, mifugo, misitu na sekta ya uvuvi nchini.

Hayo yamebainishwa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe.Laurent Luswetula (Mb), alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Ilemela, Mhe. Kafiti William Kafiti, aliyetaka kujua wakati ambao Serikali itakamilisha Kanuni hizo ili kuongeza na kupatikana kwa kinga kwa wakulima na mazao mbalimbali.

Mhe. Luswetula alisema kuwa, Serikali kupitia Wizara ya Fedha inaendelea na utafiti na maboresho katika Sekta ya Bima ya Kilimo ili kuhakikisha mfumo huo unakuwa shirikishi na wenye kuvutia uwekezaji kwa wadau wa ndani na nje ya nchi.

“Serikali inaendelea na utafiti kuhusu bima katika mnyororo wa kilimo (mazao, mifugo, misitu na uvuvi) ili pamoja na mambo mengine kuwa na Kanuni zinazovutia uwekezaji katika bima ya kilimo na kuweka mazingira wezeshi kwa wakulima ili kupata huduma za bima kwa urahisi na haraka”, alisema Mhe. Luswetula.

Aliongeza kuwa, Serikali inakusudia kuhakikisha kanuni hizo zinakuwa rafiki kwa wakulima na wakati huo huo zikichochea ushiriki wa sekta binafsi katika kutoa huduma za bima ya kilimo nchini.

Aidha, alisisitiza kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wa sekta ya bima kuhakikisha mfumo huo unakuwa endelevu na unaonufaisha wakulima kwa upana zaidi.

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), akijibu swali la Mbunge wa Ilemela, Mhe. Kafiti William Kafiti, aliyetaka kujua ni lini lini Serikali itakamilisha Kanuni za Bima ya Kilimo ili kuongeza na kupatikana kwa kinga kwa wakulima na mazao mbalimbali, bungeni jijini Dodoma. (Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha)

Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Dodoma imeendelea kusogeza huduma zake karibu na wananchi kupitia Ofisi Inayotembea, hatua inayolenga kurahisisha upatikanaji wa huduma za kodi na kuwasaidia walipakodi kutimiza wajibu wao kwa ufanisi.

Akizungumza wakati wa utoaji wa huduma hizo, Meneja wa TRA Mkoa wa Dodoma, Pendolake Elinisafi, amesema Ofisi Inayotembea ni sehemu ya mkakati wa TRA wa kuwafikia wananchi moja kwa moja katika maeneo yao ili kuwapatia huduma mbalimbali za kikodi bila kulazimika kufika katika ofisi za Mamlaka ya Mapato Tanzania.

Ameeleza kuwa huduma zinazotolewa kupitia Ofisi Inayotembea ni pamoja na usajili wa Namba za Utambulisho wa Mlipakodi (TIN), utoaji wa elimu ya kodi, ushauri wa masuala mbalimbali ya kikodi pamoja na utatuzi wa changamoto zinazowakabili walipakodi.

Elinisafi amewahimiza wananchi na wafanyabiashara wa Mkoa wa Dodoma kutumia fursa hiyo kwa kujitokeza kwa wingi ili kupata huduma na maelezo sahihi yatakayowawezesha kutekeleza wajibu wao wa kulipa kodi kwa maendeleo ya taifa.

Makamu Mwenyekiti wa Soko la Wazi la Machinga Complex, Shaban Simba, amesema Ofisi Inayotembea imekuwa na mchango mkubwa katika kurahisisha upatikanaji wa TIN na namba za malipo (Control Number), jambo ambalo limewawezesha wafanyabiashara kulipa tozo za uendeshaji wa soko kwa urahisi na kwa wakati.

Aidha, amesema huduma hiyo imechangia kubadilisha mtazamo wa baadhi ya wafanyabiashara ambao hapo awali walikuwa na uelewa mdogo kuhusu masuala ya kodi, huku ikiwasaidia kufahamu wajibu wao na namna utozaji wa kodi unavyofanyika kwa mujibu wa sheria.

Naye mfanyabiashara wa soko hilo, Tatu Bilimo, amesema kuwa uwepo wa Ofisi Inayotembea umewarahisishia kupata huduma muhimu za kikodi moja kwa moja katika maeneo yao ya biashara, hivyo kuokoa muda na gharama walizokuwa wakitumia kufuata huduma hizo katika ofisi za TRA.

Wafanyabiashara hao wameiomba TRA kuendelea kutoa huduma hiyo, wakieleza kuwa itachochea ushiriki mkubwa zaidi wa wafanyabiashara katika mfumo rasmi wa kodi na kuongeza mchango wao katika kukuza mapato ya Serikali na maendeleo ya taifa kwa ujumla.



Na Mwandishi wetu,Unguja

Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya katika kuongeza jitihada za kuweza kuongeza ufanisi mkubwa katika saula zima la uwajibikaji na kujinza mambo mbali mbali imeamua kwenda kufanya ziara maalumu ya kikazi Zanibar katika visiwa vya eneo la Unguja ambayo itaweza kuwasaidia watendaji pamoja na madiwani katika kuongeza weledi na utekelezaji wa majukumu yao mbali mbali ya kila siku.

Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya Mbeya Bi. Erica Yegella amebainisha kwamba katika ziara hiyo wameambatana na baadhi ya watendaji pamoja na madiwani mbali mbali kwa lengo la kuweza kwenda kujifunza mafunzo mbali mbali kwa kioindi cha siku nne ambayo yataweza kuwasaidia katika suala zima la utekelezaji wa majukumu yao ya kikazi ya kila siku.

Yegella amesema kwamba lengo kubwa la Rais wa awamu ya sita Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuwahudumia wananchi wake na kuleta chachu ya maendeleo na mabadiliko makubwa katika nyanja mbali mbali hivyo ana imani kwamba kufanyika kwa ziara hiyo kwa upande wa madiwani itawezamkuleta tija na mkombozi mkubwa kwa wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya kutokana na mafunzo ambayo watajifunza.

"Nashukuru sana mimi pamoja na baadhi ya waatendaji pamoja na madiwani wangu wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya tumefika salama na tumepokelewa vizuri sana Zanzibar na kwamba tumekuja maalumu kwa ajili ya ziara ya kikazi ya siku nne ambapo tutakuwepo katika maeneo mabali mbali ya Unguja na wenyeji wetu akiwemo Mkurugenzi mtendaji wa mjini magharibi ametupokea kwa heshima zote,"amebainisha Bi. Yegella.

Kadhalika Mkurugenzi huyo amesema katika ziara hiyo wataweza kupata fursa ya kujifunza masuala mbali mbali na kubadilishana uzoefu katika kutekeleza majukumu yao ikiwe pamoja na kutembelea miradi mbali mbali ya maendeeleo kwa ajili ya kujifunza jinsi wanavyoweka mikakati katika kutekeelza miradi hiyo.

Kwa upande wake Mkurugenzi mtendaji wa Manispaa ya mjini Magharibi Bi. Sabra Machano amesema kwamba amefarijika sana na ujio wa ziara hiyo kutoka kwa uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya na kuahidi kuwapa ushirikiano wa hali na mali katika kipindi chote watakapokuwa katika ziara ya mafunzo hayo.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya BI. Aiddah Haule amesema kwamba mafunzo ambayo watayapata wakiwa katika visiwa hivyo vya unguja yeye pamoja na jopo la madiwani pamoja na mkurugenzi wapo yatakuwa ni mkombozi mkubwa katika kuleta mageuzi katika nyanja mbali mbali ikiwa ni pamoja na kuwahudumia wananchi katika maeneo yao mbali mbali.






Na Janeth Raphael MichuziTv .

Serikali imezindua rasmi programu ya Grand Challenges Tanzania, jukwaa jipya la kitaifa litakalolenga kuimarisha utafiti, sayansi, teknolojia na ubunifu kwa lengo la kupata suluhu endelevu za changamoto zinazoikabili jamii katika sekta mbalimbali za maendeleo nchini.

Uzinduzi huo umefanyika jijini Dodoma ambapo Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir, amemwakilisha Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, amesema mpango huo unafungua fursa mpya kwa watafiti, wabunifu na taasisi za Kitanzania kuibua na kuendeleza teknolojia pamoja na tafiti zenye matokeo yatakayoboresha maisha ya wananchi na kuchochea maendeleo ya Taifa.

Aidha, amesema uzinduzi wa programu hiyo unaendana na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayotambua nafasi ya sayansi, teknolojia, utafiti na ubunifu kama nguzo muhimu za maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Pia aliipongeza Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), The Science for Africa Foundation, Taasisi ya Afya ya Ifakara pamoja na washirika wengine wa maendeleo kwa kushirikiana kuanzisha mpango huo.

Kwa upande wa Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH, Dkt. Amos Nungu, amesema kila kizazi hukabiliwa na changamoto zake, huku kizazi cha sasa kikikabiliwa na masuala ya usalama wa chakula, afya, ajira kwa vijana, uhifadhi wa mazingira na matumizi ya fursa zinazotokana na mapinduzi ya kidijitali. Alisisitiza kuwa wataalamu, taasisi za utafiti na wabunifu wa Tanzania wanapaswa kuwa mstari wa mbele katika kubuni suluhisho zinazolingana na mazingira na mahitaji ya nchi.

Dkt. Nungu amesema Grand Challenges Tanzania inalenga kuwakutanisha watafiti, wabunifu, watunga sera, sekta binafsi, washirika wa maendeleo na jamii kwa ujumla ili kushirikiana kutafuta majibu ya changamoto zinazowagusa wananchi moja kwa moja. Kwa mujibu wake, mafanikio ya jukwaa hilo yatategemea uwezo wa kubadilisha maarifa yanayotokana na tafiti na ubunifu kuwa matokeo yenye manufaa kwa wananchi.

Amebainisha kuwa Tanzania tayari imeweka msingi imara katika sekta ya sayansi na teknolojia kupitia uwekezaji uliofanyika kwa miaka kadhaa. Zaidi ya shilingi bilioni 129 zimehamasishwa kupitia Mfuko wa Taifa wa Kuendeleza Sayansi na Teknolojia kwa ajili ya kusaidia tafiti, maendeleo ya teknolojia, ubunifu na miundombinu ya kisayansi, huku Serikali ikichangia zaidi ya shilingi bilioni 85. Uwekezaji huo umewezesha kuanzishwa kwa maabara, vituo vya ubunifu na programu za kuwajengea uwezo watafiti pamoja na vijana wabunifu.

Sambamba na uzinduzi huo, COSTECH imetangaza kuwa itazindua Wito wa Kwanza wa Utafiti wa Grand Challenges Tanzania utakaowapa nafasi watafiti na wabunifu kuwasilisha mawazo bunifu yenye uwezo wa kutoa suluhisho kwa changamoto halisi za maendeleo. Kipaumbele kitawekwa kwa miradi inayohusisha ushirikiano wa taaluma mbalimbali pamoja na ushiriki wa vijana watafiti, wabunifu chipukizi, wanawake wanasayansi na taasisi kutoka maeneo mbalimbali ya nchi.

Serikali imeeleza kuwa mafanikio ya Grand Challenges Tanzania yatapimwa kwa kiwango ambacho tafiti na ubunifu vitachangia kuboresha afya, ustawi wa jamii, usalama wa chakula, uhifadhi wa mazingira na ukuaji wa uchumi, huku ikitoa wito kwa wadau wa sekta za umma na binafsi kuendelea kushirikiana kuendeleza ajenda ya sayansi, teknolojia na ubunifu nchini.







Na Mwandishi Wetu, Uswisi

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu ameongoza ujumbe wa Tanzania kushiriki katika Mkutano Mkuu wa 114 wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) unaofanyika Jijini Geneva, nchini Uswisi.

Akizungumza leo Juni 4, 2026 Waziri Sangu amesema mkutano huo umekuwa na manufaa makubwa kwa Taifa katika kujadili masuala ya haki za wafanyakazi, kusimamia viwango vya kazi ili kuwa na stahiki kulingana na makubaliano ya pamoja chini ya Shirika la Kazi Duniani.

Amebainisha maeneo makuu ya mjadala katika mkutano huo wa mwaka 2026 ni Masuala mbalimbali yanayohusu Sekta ya Kazi Duniani, Utekelezaji wa mikataba mbalimbali ambayo Tanzania imeridhia chini ya ILO na Matumizi ya Akili Unde (AI) inavyoweza kutumika katika kuhakikisha kazi za staha zinazingatiwa kwa wafanyakazi.

Pia amesema kuwa katika mkutano huo wameweza kujadili na Wadau wa Utatu (Serikali, Waajiri na Wafanyakazi) kutoka Tanzania Bara na Visiwani ili kuona namna bora ya kushirikiana na kuwa na majadiliano ya kijamii ambayo yanaleta tija hususan katika nyakati hizi za matumizi ya teknolojia na ukuaji wa uchumi wa kidijitali.

Wakati huo huo Waziri Sangu amemshukuru Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuruhusu wadau wa utatu kushiriki katika mkutano huo ambao unawawezesha kubadilishana uzoefu na kujadili masuala yanayohusu ustawi wa sekta ya kazi.

Mkutano Mkuu wa 114 wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) unaofanyika Jijini Geneva, nchini Uswisi unashirikisha wawakilishi wa Serikali, Waajiri na Wafanyakazi kutoka nchi wanachama 187. Mkutano huo ulianza rasmi tarehe 1 Juni, 2026 na utahitimishwa Juni 12, 2026.




Na Farida Mangube Morogoro

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimesisitiza umuhimu wa kuwekeza katika tafiti, ubunifu na teknolojia za uzalishaji wa mbegu bora ili kuongeza tija katika sekta ya kilimo na kuimarisha usalama wa chakula nchini.

Kauli hiyo imetolewa wakati wa mjadala wa masuala ya uwekezaji katika miradi ya maendeleo ya uzalishaji wa mbegu na ubunifu wa teknolojia za kilimo ulioandaliwa na SUA kwa kushirikisha wadau mbalimbali wa sekta ya kilimo, wakiwemo watafiti, taasisi za kifedha, wazalishaji wa mbegu na Taasisi ya Kudhibiti Ubora wa Mbegu Tanzania (TOSCI).

Akizungumza kwa niaba ya Makamu Mkuu wa SUA, Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Taaluma, Utafiti na Ushauri wa Kitaalam Prof. Maulid Mwatawala alisema maendeleo ya sekta ya kilimo yanategemea kwa kiwango kikubwa uwekezaji katika teknolojia rahisi, tafiti na ubunifu unaolenga kutatua changamoto zinazowakabili wakulima.

Alisema matumizi ya teknolojia na mbegu bora yanaweza kuongeza uzalishaji wa mazao, kupunguza gharama za uzalishaji na kuwasaidia wakulima kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi, hivyo kuna haja ya kuendelea kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi za utafiti, Serikali na sekta binafsi.

Profesa Mwatawala alieleza kuwa SUA itaendelea kutoa mchango wake katika kuzalisha maarifa, teknolojia na wataalamu watakaosaidia kuendeleza sekta ya kilimo na kuhakikisha matokeo ya tafiti yanawafikia wakulima kwa wakati.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TOSCI, Bw. Nyasebwa Chimagu, alisema taasisi hiyo imejipanga kuimarisha ukaguzi katika maeneo mbalimbali ya uzalishaji na usambazaji wa mbegu ili kuhakikisha wakulima wanapata mbegu zilizothibitishwa na zenye ubora unaotakiwa.

Alisema uuzaji wa mbegu feki unahatarisha mafanikio ya wakulima na unaweza kusababisha hasara kubwa katika uzalishaji wa mazao, jambo linaloweza kuathiri juhudi za taifa katika kuhakikisha upatikanaji wa chakula cha kutosha.

“Hatutasita kuchukua hatua kali kwa mtu yeyote atakayebainika kukiuka sheria za uzalishaji na uuzaji wa mbegu. Tunataka kulinda maslahi ya wakulima na kuhakikisha wanapata mbegu bora zinazowezesha kuongeza uzalishaji,” alisema Bw. Chimagu.

Nae Mkurugenzi wa Mipango, Ushauri na Mahusiano wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB), Bw. Mkani Waziri, alisema kuna umuhimu wa mifumo ya sekta ya kilimo kuunganishwa kidijitali ili kurahisisha upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wakulima.

Alisema matumizi ya mifumo ya kidijitali yatawawezesha wakulima kupata mikopo na huduma nyingine za kifedha kwa urahisi zaidi bila kujali mahali walipo, hatua itakayochochea ukuaji wa sekta ya kilimo na kuongeza ushiriki wa wakulima katika uchumi wa kisasa.

Wadau waliohudhuria mjadala huo walikubaliana kuwa uwekezaji katika mbegu bora, teknolojia za kisasa, tafiti za kilimo na huduma za kifedha ni nguzo muhimu katika kuifanya sekta ya kilimo kuwa yenye tija, ushindani na mchango mkubwa katika maendeleo ya uchumi wa nchi.




Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ametembelea banda la Benki ya NMB katika Tamasha la Uwekezaji Zanzibar 2026 lililofanyika Golden Tulip Airport Hotel, Zanzibar.

NMB ilikuwa miongoni mwa wadhamini wa tamasha hilo la kila mwaka lililowakutanisha viongozi wa serikali, wawekezaji, taasisi za fedha, watendaji wakuu na wadau wa sekta binafsi kujadili fursa za uwekezaji na ukuaji endelevu wa uchumi wa Zanzibar.

Rais Dkt. Mwinyi alipokelewa na Meneja wa Benki ya NMB, Tawi la Zanzibar, Ahmed Nassor, ambaye alimweleza kuhusu suluhisho mbalimbali zinazopatikana kupitia NMB kwa wawekezaji, kampuni na taasisi zinazofanya kazi Zanzibar.

Akizungumza katika banda hilo, Nassor alisema ushiriki wa NMB katika tamasha hilo unaonesha utayari wa benki hiyo kuendelea kuwa mshirika wa karibu wa Serikali na sekta binafsi katika kuchochea ukuaji wa uchumi wa Zanzibar.

“Kwa NMB, Tamasha la Uwekezaji Zanzibar ni jukwaa muhimu la kuonesha suluhisho tulizonazo kwa wawekezaji, makampuni na taasisi zinazofanya kazi Zanzibar. Tupo tayari kusaidia mahitaji yao ya kifedha kupitia huduma za kibenki, malipo, makusanyo na mifumo ya kidijitali, huku tukiendelea kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kusukuma mafanikio makubwa zaidi ya kiuchumi kwa Zanzibar,” alisema Nassor.



















Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) imezindua kampeni maalum inayofahamika kama “Tunakuona Mbali”, ikiwa ni sehemu ya jitihada zake za kuwawezesha Watanzania kutoka makundi mbalimbali ya kijamii kufikia malengo yao ya maendeleo kupitia huduma rasmi za kifedha.

Kampeni hiyo inalenga kuhamasisha utamaduni wa kuweka akiba, kuwekeza, kutumia huduma za kifedha kwa usahihi na kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu fursa zinazotolewa na benki katika kuboresha maisha yao. Kupitia kampeni hiyo, NBC inalenga kuwafikia wafanyakazi, wakulima, watoto, vijana, wanafunzi, wanawake, wastaafu, vikundi vya kijamii, taasisi za dini, Watanzania wanaoishi nje ya nchi pamoja na wafanyabiashara wadogo, wakati, na wakubwa.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni hiyo uliofanyika katika makao makuu ya benki hiyo jijini Dar es Salaam mapema leo, Mkuu wa Kitengo cha Masoko wa NBC, Bw. David Raymond, alisema kampeni hiyo imejengwa juu ya falsafa ya kutambua na kuunga mkono ndoto na juhudi za Watanzania katika hatua mbalimbali za maisha yao.

“Tunaposema ‘NBC Tunakuona Mbali’, tunamaanisha kuwa tunakupa zaidi ya huduma za kawaida za benki. Tunatambua kwamba kila Mtanzania ana ndoto na malengo ya kufikia mafanikio katika maisha yake; iwe ni kujenga nyumba, kukuza biashara, kusomesha watoto, kuanzisha uwekezaji au kujijengea usalama wa kifedha kwa sasa na siku zijazo. Ndiyo maana, kama taasisi ya kifedha, tunajiona kuwa mshirika wa safari hiyo ya maendeleo.

Akaunti ya NBC ni zaidi ya mahali pa kuhifadhi fedha; ni suluhisho kamili la kifedha mfano wa ‘wallet’ inayokuwezesha kufanya miamala ya kila siku kwa urahisi,ni mahali pa kuweka akiba, kutuma na kupokea pesa, kupata mikopo, kuwekeza katika masoko ya hisa na mifuko ya uwekezaji, pamoja na kuendesha biashara yako kwa ufanisi zaidi. Kupitia huduma hizi, tunalenga kukupa nyenzo na fursa zinazokusaidia kufikia malengo yako na kutimiza ndoto zako,” alisema.

Aliongeza kuwa maendeleo ya mtu mmoja mmoja yana mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi wa taifa. Hivyo, kuwasaidia wananchi kupata elimu sahihi ya fedha, kuweka akiba, kuwekeza na kutumia huduma rasmi za mikopo ni njia muhimu ya kujenga uchumi jumuishi unaowanufaisha wengi zaidi.

“Kila tunapomsaidia mfanyabiashara kukuza mtaji wake, mkulima kuongeza uzalishaji, mzazi kuandaa mustakabali wa mtoto wake au kijana kuanza safari yake ya kifedha, tunakuwa pia tunachangia ukuaji wa uchumi wa nchi. Hiyo ndiyo maana halisi ya kuwaona Watanzania wakifika mbali,” alisisitiza.

Kupitia kampeni hiyo, NBC itatoa elimu ya kifedha na kuhamasisha matumizi ya bidhaa na huduma zake mbalimbali zilizobuniwa kulingana na mahitaji ya makundi tofauti ya kijamii. Miongoni mwa huduma hizo ni Akaunti ya Chanua kwa watoto, Akaunti ya Malengo, Akaunti ya Johari kwa wanawake, Akaunti ya Mwalimu, Akaunti ya Mshahara, Akaunti ya Wajasiriamali, Akaunti ya Waalimu, Akaunti ya Wanafunzi, Akaunti ya Kua Nasi, Akaunti ya Vikundi, Akaunti Binafsi, Akaunti ya Diaspora pamoja na Akaunti za Biashara pamoja na akaunti ya Muda Maalum kwa ajili ya uwekezaji.

Kwa upande wake, Meneja wa Bidhaa na Mauzo wa NBC, Bi. Dorothea Mabonye, alisema kampeni hiyo pia itatoa elimu kuhusu usimamizi wa fedha, matumizi sahihi ya mikopo, huduma za bima, mifumo ya malipo na miamala ya kidigitali ili kuwajengea wananchi uwezo wa kufanya maamuzi bora ya kifedha.

“Kupitia kampeni hii tunataka kuwasaidia Watanzania kutambua kuwa huduma za kifedha si kwa ajili ya kutunza fedha pekee, bali ni nyenzo muhimu ya kufikia malengo yao ya maisha. Tunataka kuona wananchi wakitumia huduma hizi kujenga msingi imara wa maendeleo yao na ya familia zao,” alisema.

Alifafanua kuwa huduma mbalimbali zinazotolewa na benki hiyo zimebuniwa ili kukidhi mahitaji ya kila kundi. “Kwa mfano, wazazi wanaweza kuwawekea watoto wao msingi wa utamaduni wa kuweka akiba kupitia Akaunti ya Chanua huku wafanyakazi pia wakiweza kupata mkopo wa muda mfupi unaowasaidia kukidhi mahitaji ya dharura wanaposubiri muda wa kupokea mshahara’’ alisema

Aliongeza kuwa kupitia akaunti ya Diaspora Watanzania waishio nje ya nchi wanaweza kupata fursa rahisi za kuwekeza na kushiriki maendeleo ya nchi kupitia mikopo ya nyumba na akaunti ya muda maalum ya uwekezaji.

Naye Mkuu wa Huduma za Kidigitali wa NBC, Bw. Ulrik Peter, alisema teknolojia imeendelea kuwa daraja muhimu la kuwafikishia wananchi huduma za kifedha kwa haraka, kwa gharama nafuu na bila vikwazo vya umbali.

Alisema NBC imeendelea kuwekeza katika mifumo ya kidigitali kama vile NBC Kiganjani, NBC Connect, huduma za kadi za benki na mawakala ili kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanapata huduma za kifedha bila kulazimika kutembelea matawi ya benki.

“Ujumuishaji wa kifedha hauwezi kufikiwa bila matumizi makubwa ya teknolojia. Kupitia kampeni hii tunawahamasisha wananchi kutumia huduma za kidigitali ambazo zinawawezesha kuokoa muda, kupunguza gharama za miamala na kupata huduma za kifedha popote walipo, wakati wowote na kwa namna wanayohitaji kufanya matumizi yao ya kila siku,” alisema.

Aliongeza kuwa uwekezaji uliofanywa na NBC katika mifumo ya kidigitali na utoaji wa kadi papo hapo kwa wateja wanaofungua akaunti mpya ni sehemu ya mkakati wa kuondoa vikwazo vinavyoweza kuwazuia wananchi kushiriki kikamilifu katika uchumi rasmi na kukua kiuchumi.



Maofisa mbalimbali wa Benki ya NBC wakiongozwa na Mkuu wa Bidhaa na Mauzo, Bw. Abel Kaseko (kushoto) wakipeperusha bendera kuashiria uzinduzi wa kampeni maalum inayofahamika kama “Tunakuona Mbali”, ikiwa ni sehemu ya jitihada za benki hiyo kuwawezesha Watanzania kutoka makundi mbalimbali ya kijamii kufikia malengo yao ya maendeleo kupitia huduma rasmi za kifedha. Hafla ya uzinduzi wa kampeni hiyo imefanyika leo jijini Dar es Salaam.

Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma

Spika wa Bunge, Mussa Azan Zungu, ametoa onyo dhidi ya tabia ya utoro miongoni mwa baadhi ya wabunge na viongozi wa Serikali, akisema hali hiyo imezidi na kuanza kudhoofisha nidhamu pamoja na ufanisi wa shughuli za Bunge.

Akizungumza leo Bungeni jijini Dodoma, Spika Zungu amesema baadhi ya wabunge wamekuwa wakifika asubuhi kusaini mahudhurio kisha kuondoka, na baadaye kurejea jioni kwa ajili ya kusaini tena bila kushiriki vikao vya Bunge.

Amesema pia kuna wabunge wanaosaini mahudhurio kwa niaba ya wenzao ambao hawapo kabisa Bungeni, jambo alilolitaja kuwa ni ukiukwaji wa taratibu za Bunge unaostahili kuchukuliwa hatua za kisheria na kinidhamu.

“Kuna wanaokuja asubuhi, wanasaini na kuondoka. Jioni wanarudi kusaini tena. Wapo pia wanaowasainia wenzao ambao hawapo. Tunawafahamu wanaosaini na wanaosainiwa, na hatua za kibunge zinapaswa kuchukuliwa,” alisema Spika Zungu.

Aidha, amesema kuna kundi lingine la wabunge ambao hawaonekani kabisa katika shughuli za Bunge licha ya kutokuwa na sababu za msingi za kutokuwepo, hali aliyoeleza kuwa ni kudharau mamlaka ya Spika pamoja na wananchi waliowachagua.

Spika Zungu amesisitiza kuwa kuanzia Jumatatu ijayo hatarajii kuona tabia hizo zikiendelea, akibainisha kuwa Ofisi ya Katibu wa Bunge ina uwezo wa kufuatilia na kubaini mahali alipo kila mbunge wakati wa shughuli za Bunge.

Pia aliiagiza Wizara inayosimamia mawasiliano kushirikiana katika kuimarisha mifumo ya ufuatiliaji wa mahudhurio ya wabunge ili kudhibiti utoro huo.

Katika hatua nyingine, Spika alimwelekeza Waziri Palamagamba Kabudi kulifanyia kazi suala hilo kwa kuwa liko chini ya usimamizi wa ofisi yake.

Vilevile, alikemea utaratibu wa baadhi ya mawaziri na manaibu wao kuwa safarini kwa wakati mmoja, akisema hali hiyo husababisha kukosekana kwa uwakilishi wa Serikali ndani ya Bunge.

“Haipendezi Waziri kuwa kwenye ziara huku Naibu Waziri naye akiwa kwenye ziara wakati huohuo. Wapeane zamu ili mmoja awepo Bungeni wakati mwingine akiwa kwenye majukumu ya nje,” alisisitiza.

Kauli ya Spika imekuja wakati Bunge likiendelea na shughuli zake jijini Dodoma, huku akitaka nidhamu ya mahudhurio irejee na kila kiongozi kutimiza wajibu wake kwa wananchi.



Na Mwandishi Wetu, Dodoma
MKURUGENZI Mtendaji wa Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP Centre), David Kafulila, amesema mfumo wa ubia kati ya sekta ya umma na sekta binafsi (PPP) una mchango mkubwa katika kuongeza ufanisi wa taasisi za umma na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.

Kafulila alitoa kauli hiyo jana wakati akizungumza katika mhadhara wa umma uliofanyika katika Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), akieleza kuwa mataifa mengi duniani yameendelea kuwekeza katika mfumo wa PPP kutokana na manufaa yake katika kuimarisha utendaji wa taasisi na kuongeza tija ya kiuchumi.

Alisema sababu kuu tatu zinazochochea matumizi ya mfumo huo duniani ni kuvutia mitaji ya sekta binafsi katika utekelezaji wa miradi ya umma, kuongeza ufanisi wa taasisi za serikali na kukuza ubunifu.

“PPP siyo tu njia ya kupata fedha za kutekeleza miradi ya maendeleo, bali ni nyenzo muhimu ya kuongeza ufanisi wa taasisi za umma na kuhamasisha ubunifu unaochangia maendeleo endelevu ya uchumi,” alisema Kafulila.

Alibainisha kuwa tafiti mbalimbali zinaonesha kuwa katika baadhi ya nchi zilizoendelea, takribani asilimia 25 ya utajiri wa taifa unatokana na ufanisi wa taasisi zake, huku rasilimali za asili zikichangia karibu asilimia tano pekee.

Kwa mujibu wa Kafulila, mafanikio ya nchi hizo hayatokani na ukosefu wa rasilimali za asili, bali uwezo wa kujenga mifumo madhubuti inayowezesha matumizi bora ya rasilimali zilizopo.

Alitolea mfano nchi za China, Marekani na Urusi ambazo pamoja na kuwa na utajiri mkubwa wa rasilimali za asili, zimejikita zaidi katika kuimarisha rasilimali watu, ubunifu na taasisi zenye ufanisi mkubwa.

“China inazalisha dhahabu nyingi kuliko nchi yoyote Afrika, Marekani ina mafuta mengi kuliko mataifa mengi duniani na Urusi ina gesi nyingi kuliko nchi yoyote Afrika. Hata hivyo, msingi wa maendeleo yao ni nguvu ya taasisi, ubunifu na rasilimali watu,” alisema.

Kafulila alisisitiza kuwa Tanzania inaweza kunufaika zaidi na mfumo wa PPP kwa kutumia sekta binafsi kama mshirika wa maendeleo katika utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati, huku ikiimarisha ufanisi wa taasisi za umma na kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi.

Top News