Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Mhe. Edward Mpogolo, amefanikiwa kumaliza mgomo wa wafanyakazi zaidi ya 1,500 wa Kiwanda cha NAMERA kilichopo Gongolamboto, jijini Dar es Salaam, mgomo uliokuwa umeanza tarehe 16 Januari, 2026.

Mgomo huo ulitokana na madai ya mishahara, ambapo mshahara wa kima cha chini kwa sekta binafsi umewekwa kwa mujibu wa Tangazo na Amri ya Serikali Namba 605A ya tarehe 13 Oktoba, 2025, inayotoa ongezeko la wastani wa asilimia 33.4. Kutokana na ongezeko hilo, mshahara wa chini umeongezeka kutoka Shilingi 275,060 mwaka 2022 hadi Shilingi 358,222 mwaka 2025. Hivyo basi, hakuna mtu au taasisi yoyote inayoruhusiwa kulipa mshahara chini ya kiwango kilichobainishwa katika Amri hiyo ya Serikali, hata kwa kuwepo kwa makubaliano yoyote kati ya taasisi binafsi kupitia chama chao cha waajiri (ATE) au mifumo mingine ya ndani.

Akizungumza na wafanyakazi pamoja na uongozi wa kiwanda hicho, Mhe. Mpogolo amesisitiza kuwa Amri ya Serikali ni ya lazima kutekelezwa na kwamba hakuna kampuni, taasisi au mwajiri yeyote anayekubalika kushuka chini ya viwango vilivyowekwa kisheria. Ameeleza kuwa makubaliano yoyote hayawezi kwenda kinyume na Amri ya Serikali.

Mpogolo ametoa maelekezo muhimu kwa uongozi wa kiwanda na wafanyakazi, ikiwemo kuhakikisha malipo ya mishahara yanatolewa kwa mujibu wa Tangazo la Serikali Na. 605A la mwaka 2025, huku akisisitiza kuwa hakuna mfanyakazi atakayefukuzwa kutokana na kushiriki mgomo, ili kuimarisha mahusiano bora kati ya mwajiri na waajiriwa. Aidha, ameitaka kiwanda kushirikiana na Chama cha Wafanyakazi (TUICO) na Afisa Kazi wa Mkoa wa Dar es Salaam kufanyika uchaguzi wa viongozi wa wafanyakazi watakao kuwa kiungo madhubuti kati ya wafanyakazi na uongozi, pamoja na kupitia mikataba ya ajira kuhakikisha inakidhi sheria na kanuni zinazohitajika. Mpogolo pia amehimiza ujenzi wa mahusiano mazuri na kulinda kiwanda kutokana na mchango wake mkubwa katika uchumi wa taifa na nafasi zake muhimu za ajira kwa wananchi.

Kwa upande wao, wafanyakazi wa kiwanda hicho wameeleza kuridhishwa na hatua zilizochukuliwa na Mkuu wa Wilaya, wakisema kuwa zimeleta matumaini mapya na kurejesha amani kazini. Wameahidi kurejea kazini mara moja na kuendelea kutekeleza majukumu yao kama kawaida.

Naye Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dar es Salaam (RPC), ACP Yustino Mgonja, amepongeza juhudi za Mhe. Mpogolo katika kushughulikia mgogoro huo kwa haraka na kwa busara. ACP Mgonja amesema hali ya usalama katika eneo la kiwanda ni shwari na amewahakikishia wafanyakazi kuwa wapo salama.

Kwa upande wake, mmiliki wa Kiwanda cha NAMERA amesema yupo tayari kutekeleza makubaliano yote yaliyofikiwa kati ya uongozi wa kiwanda na Serikali, huku akiahidi kuboresha mazingira ya kazi na kuimarisha ushirikiano kati ya waajiri na wafanyakazi kwa maslahi ya pamoja.

Dc. Mpogolo amesema kuwa kiwanda hicho ni muhimu sana, hasa katika upande wa ajira. Hivyo basi, migogoro inaweza kuharibu upatikanaji wa ajira na ukuaji wa uchumi, kwa hivyo migogoro si jambo zuri.

Kufuatia kumalizika kwa mgomo huo, shughuli za uzalishaji katika Kiwanda cha NAMERA zinatarajiwa kurejea kama kawaida, huku wafanyakazi wakirejea kazini wakiwa na ari mpya ya kufanya kazi.



Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo, ameitaka Wakala wa Vipimo (WMA) nchini kuongeza uwajibikaji katika kusimamia kikamilifu utekelezaji wa Sheria ya Vipimo ili kuwalinda walaji dhidi ya udanganyifu na kuhakikisha wanapata bidhaa na huduma kulingana na thamani halisi ya fedha zao.

Londo amesema usimamizi madhubuti wa vipimo ni msingi muhimu katika kujenga uchumi shindani, himilivu na jumuishi, sambamba na kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050.

Ameyasema hayo wakati wa ziara ya kikazi katika Ofisi za Wakala wa Vipimo katika Kituo cha Uhakiki wa Vipimo Misugusugu Mkoa wa Pwani, ambapo amesisitiza kuwa Wizara ya Viwanda na Biashara imejipanga kuhakikisha kunakuwepo na mazingira wezeshi ya biashara huku ikijenga imani kwa walaji katika huduma na bidhaa wanazopata.

Naibu Waziri ameongeza kuwa kutokuwepo kwa usimamizi sahihi wa vipimo kunawanyima walaji haki zao za msingi na kudhoofisha ushindani wa haki katika biashara, jambo linaloweza kuathiri ukuaji wa uchumi kwa ujumla.

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Vipimo Bw. Alban Kihulla amewasihi Wananchi kushirikiana na Wakala huo kwa kutoa taarifa pindi wanapobaini kupatiwa huduma kwa kutumia vipimo visivyo sahihi, akisema ushirikiano wa Wananchi ni nyenzo muhimu katika kudhibiti vitendo vya udanganyifu na kuimarisha haki katika biashara.

Wakala wa Vipimo ina jukumu la kuhakikisha vipimo vinavyotumika katika biashara vinakuwa sahihi kwa mujibu wa Sheria, hatua inayolenga kulinda maslahi ya walaji na kukuza biashara nchini.






Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Dkt. Islam Seif Salum (kulia) akizungumza na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Richard Muyungi muda mfupi baada ya kuwasili katika Ofisi hizo Mjini Zanzibar leo Alhamisi Januari 22, 2026.

*********************

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar zimepanga kuimarisha mashirikiano ili kuhakikisha fursa za Muungano zinawanufaisha wananchi na kuakisi maono ya Waasisi.

Hayo yamesemwa leo Alhamisi (Januari 22, 2026) Mjini Zanzibar na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Richard Muyungi wakati wa ziara yake aliyoifanya kwa Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar kwa ajili ya kujitambulisha.

Dkt. Muyungi amesema Serikali zote mbili zimekuwa mstari wa mbele katika kutatua hoja za Muungano hatua inayolenga katika kufungua fursa za kijamii, kiuchumi na kiutamaduni kwa wananchi wa Tanzania Bara na Zanzibar.

“Waasisi wetu walikuwa na malengo ya kubainisha fursa za mashirikiano ziweze kuwanufaisha wananchi, hivyo wakati umefika sasa wa kuhakikisha fursa hizo zinakuwa agenda muhimu tunazopaswa kuzibeba kama Watendaji wa Serikali” amesema Dkt. Muyungi.

Ameeleza kuwa ni wakati mwafaka wa kuenzi kwa matendo maono ya viongozi na waasisi wa Muungano kwa kuhakikisha wananchi wa pande zote mbili wananufaika ipasavyo kwa kufanya hivyo kutafsiri nia na malengo ya waasisi.

“Hadi sasa hoja 22 za Muungano zimepatiwa ufumbuzi, tumebaki na hoja 3 sawa na mafanikio ya asilimia 99 ya utatuzi wa hoja….ni muhimu kuhakikisha kuwa utatuzi wa hoja hizo unaleta manufaa endelevu kwa wananchi” amesema Dkt. Muyungi.

Aidha Dkt. Muyungi ameshauri kurejeshwa kwa mashindano ya michezo ya pasaka ambayo hapo awali yalikuwa ni sehemu muhimu ya kuimarisha mahusiano na mashiriano baina ya Tanzania Bara na Zanzibar.

Akifafanua zaidi Dkt. Muyungi amesema viongozi na watendaji wa serikali zote mbili wamekusudia kutangaza fursa za muungano kwa wananchi na kuwahimiza wataalamu kuchakata fursa hizo ili kuona njia bora ya kuwanufaisha wananchi.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Serikali ya Mapnduzi Zanzibar, Dkt. Islam Seif Salum Ofisi hizo zimekuwa zikishirikiana kwa karibu katika kuimarisha uratibu wa masuala ya Muungano na hatua hiyo imeendelea kuwanufaisha wananchi wa pande zote mbili.

“Katika kikao baina yetu tumekubaliana kuimarisha mashirikiano kupitia vikao vya pamoja na tumepanga wataalamu wetu kuweza kukutana ili kuandaa maazimio na kuangalia namna bora zaidi ya kuimarisha Muungano wetu” amesema Dkt. Islam.


Naibu Katibu Mkuu (Muungano) Ofisi ya Makamu wa Rais, Bw. Abdallah Hassan Mitawi akifuatila mazungumzo baina ya Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Richard Muyungi na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Dkt. Islam Seif Salum leo Alhamisi Januari 22, 2026 Mjini Zanzibar.

Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar Dkt. Islam Seif Salum akizungumza wakati wa kikao baina yake na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Richard Muyungi wakati wa ziara yake ya kujitambulisha leo Alhamisi Januari 22, 2026 Mjini Zanzibar.

Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Dkt. Islam Seif Salum (mbele kulia) akizungumza wakati wa kikao baina yake na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Richard Muyungi wakati wa kikao baina yao kilichofanyika Mjini Zanzibar leo Alhamisi Januari 22, 2026.

Naibu Katibu Mkuu (Muungano) Ofisi ya Makamu wa Rais, Bw. Abdallah Hassan Mitawi (wa kwanza kushoto) akiwa pamoja na Mkurugenzi wa Muungano Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Juma Mohammed Salum (katikati) wakifuatilia kikao bainaya Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Richard Muyungi na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Dkt. Islam Seif Salum.

Katbu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Richard Muyungi (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Dkt. Islam Seif Salum muda mfupi baada ya kumalizika kwa kikao baina yao kilichofanyika leo Alhamisi Januari 22, 2026 Mjini Zanzibar.

Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Richard Muyungi akiongozana na Naibu Katibu Mkuu (Muungano) Ofisi ya Makamu wa Rais, Bw. Abdallah Mitawi muda mfupi baada ya kumalizika kwa kikao baina yake na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Dkt. Islam Seif Salum.

(NA MPIGAPICHA WETU)





Na Oscar Assenga,TANGA


BENKI Kuu ya Tanzania (BOT) imesema kwamba taasisi ndogo zinazotoa huduma za kubadilisha fedha za kigeni nchini zinapaswa kusajiliwa ili ziweze kupata leseni ya kuendesha shughuli zao,kinyume na hapo ni kosa kisheria.

Kauli hiyo ilitolewa leo na Afisa Mwandamizi Mkuu kutoka Kurugenzi ya Usimamizi wa Sekta ya Fedha Benki Kuu ya Tanzania (BOT) Mwile Kauzeni wakati alipokuwa akizungumzia na Waandishi wa habari kwenye viwanja vya Usagara Jijini Tanga, eneo ambalo Maadhimisho ya Wiki ya fedha kitaifa yanafanyika mwaka huu.

Mwile alikuwa akijibu Swali la Wanahabari waliotaka kujua hatua ambazo zinachukuliwa na benki kuu ya Tanzania katika kudhibiti Watu wanaoendesha biashara ya kubadilisha fedha kiholela.

Ambapo badala yake aliwasihi kufuata Sheria hatua ambayo itawawezesha kupata inayoruhusu uendeshaji kazi hiyo.

Alisema kuwa, ili mtu kufanya biashara hiyo anapaswa kufuata taratibu za kisheria kwa vile kinyume chake atakuwa ametenda kosa la jinai ambapo amewataka wale wenye nia kuendesha shughuli hiyo kutembelea matawi yake.

Aidha alisema taasisi ndogo za huduma za fedha zinahitaji kusajiliwa ili kuweza kupata leseni BOT kutokana na kwamba kubadilisha fedha bila leseni ni kosa kisheria

Awali akizungumza Afisa Mchambuzi Masuala ya Fedha wa BOT Charles Kanuda alisema kwamba, Serikali imekuja na mfuko wa udhamini wa mikopo ambapo kwa mtanzania anayehitaji mkopo huku akiwa hana dhamana toshelevu atapata dhamana mpaka asilimia 75.

Kanuda alisema kwamba,watu wengi wamekuwa wakijaribu kwenda kukopa huku wakiombwa dhamana yenye thamani kubwa zaidi ya mikopo wanayohitaji na hivyo kushindwa kupata mikopo.

Amesema kwamba hali hiyo imewasababisha watanzania walio wengi kushindwa kuchukua mikopo au kuchukua kiasi kidogo jambo ambalo limeathiri ufanisi wa biashara zao wanazoziendesha.

Katika maadhimisho haya ya wiki ya fedha kitafa yenye kauli mbiu ya " elimu ya fedha , msingi wa Maendeleo ya kijamii na kiuchumi" Wadau mbalimbali walitembelea na kupatiwa elimu banda la BOT.

Mwajuma Kileo ni Mwalimu wa Shule ya Msingi Mkwakwani Jijini Tanga, yeye alielezea kuridhishwa kwake na elimu aliyoipata baada ya kutembelea banda hilo la BOT.

Alisema kwamba, kwa kutembelea banda hilo alijifunza namna ya kutambua fedha bandia mambo ambayo pia walikuwa wakiwafundisha wanafunzi kupitia somo la uraia wanapokuwa Shule.

Adrus Mahmoud (12) mwanafunzi wa darasa la sita kwenye Shule hiyo ya Mkwakwani,alisema amefarijika kupatiwa elimu ya ziada juu ya kutambua alama za kificho zilizomo kwenye noti na hivyo kumsaidia kubaini zilizo za bandia.


Na OWM- TAMISEMI, Dodoma

Tathmini ya utekelezaji wa Mkataba wa Lishe kwa mwaka wa fedha 2024/25 imeonesha mafanikio makubwa, ambapo rangi ya kijani imetawala katika viashiria vingi vya utekelezaji, ikiwa ni ishara ya kufanya vizuri kwa mikoa na halmashauri nchini.

Hayo yamesemwa leo Januari 22,2026 jijini Dodoma na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Prof. Riziki Shemdoe, wakati akifungua mkutano wa tathmini ya utekelezaji wa Mkataba wa Lishe kwa mwaka wa fedha 2024/25.

Prof. Shemdoe amesema Taifa limeendelea kupiga hatua kubwa katika kuboresha hali ya lishe kwa wananchi, hali inayochangia kuimarisha nguvu kazi yenye afya bora na kuongeza mchango wake katika ukuaji wa uchumi wa Taifa.

“Nawashukuru Wakuu wa Mikoa, Makatibu Tawala wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, Maafisa Watendaji wa Kata, Vijiji na Mitaa pamoja na viongozi na watendaji wote wa Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Mikoa na Halmashauri kwa kazi kubwa ya kusimamia, kuratibu na kutekeleza Mkataba wa Lishe,” amesema Prof. Shemdoe.

Amewahakikishia kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI itaendelea kushirikiana na kuwapa ushirikiano wa karibu ili kuhakikisha azma ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kupunguza na hatimaye kutokomeza kabisa matatizo ya lishe nchini inafikiwa.

Amebainisha  kuwa mafanikio hayo ni sehemu ya utekelezaji wa usia wa Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, aliyehimiza kuimarishwa kwa sekta za Elimu, Afya na Uchumi ili kupambana na maadui watatu wa Taifa ambao ni ujinga, maradhi na umasikini.

Prof. Shemdoe amesema uwekezaji katika lishe ni mkakati wa kiuchumi wenye tija kubwa, na kwamba Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 imeipa kipaumbele kujenga jamii yenye afya kwa kuzingatia lishe bora ili kila mwananchi astawi.

Aidha, amesema Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2025/30, ibara ya 2.3.2 (xi), imetambua umuhimu wa lishe katika kulinda na kujenga afya za wananchi, ambapo CCM itaendelea kuhimiza na kusimamia upatikanaji wa lishe bora kwa wote.

Akizungumza kuhusu dhana ya lishe bora, Prof. Shemdoe amesema ni matokeo ya kutokuwepo kwa magonjwa mwilini pamoja na ulaji sahihi wa vyakula vyenye virutubishi vyote vinavyohitajika.

Ameongeza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita imedhamiria kuanza utekelezaji wa Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote, hatua itakayosaidia kuhakikisha wananchi wote wanapata huduma stahiki za afya na kushinda adui maradhi.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt. Seif Shekalaghe, amesema lishe ni suala la msingi katika ukuaji wa binadamu kiakili na kimwili, sambamba na kuongeza tija katika shughuli za kiuchumi na maendeleo ya Taifa kwa ujumla.

Naye,Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu  anayeshughulikia afya Prof.Tumaini Nagu amesema serikali itaendelea  kusimamia kwa karibu utoaji wa huduma za lishe katika Mikoa na Halmashauri zote nchini.









Na Mwandishi Wetu


TUNAPOINGIA Mwaka Mpya, wengi wetu hutafakari malengo yetu, matarajio, na aina ya maisha tunayotaka kuishi.

Ingawa mara nyingi tunafikiria akiba ya kifedha, ukuaji wa kazi, au maendeleo binafsi, eneo moja muhimu linalopuuzwa mara nyingi ni afya yetu.

Hayo yanaelezwa na Dk. Harold Adamson ambaye ni Ofisa Mkuu Mtendaji wa Jubilee Health Insurance wakati anaelezea Gharama ya Matibabu yaliyochelewa dhidi ya Thamani ya Bima ya Afya.

Anafafanua kwamba uangalizi huo mara nyingi husababishwa na kutokuwepo kwa mpango sahihi wa afya unaohakikisha upatikanaji wa huduma bora kwa wakati unaofaa.

"Bila hiyo, huduma za kinga huahirishwa na matibabu hucheleweshwa, na kuruhusu hali za afya ambazo zingeweza kudhibitiwa kuongezeka na kuwa kubwa na zenye gharama kubwa na inayoweza kuepukika.

"Nchini Tanzania, matibabu ya kuchelewa hubeba matokeo ya kiafya na kifedha. Kinachoanza kama ugonjwa wa kawaida kinaweza kuendelea kuwa hali mbaya inayohitaji kulazwa hospitalini, huduma maalum, au kutumia muda mrefu kupona.

" Matokeo haya yanasumbua kaya, kuharibu maisha, na kuweka shinikizo linaloweza kuepukika kwenye mifumo ya afya. Mara nyingi, gharama ya matibabu ya hatua za mwisho huzidi gharama ya kujikinga."

Akieleza zaidi anasema Bima ya Afya ya Jubilee, inaona ukweli huu kila siku kupitia ushirikiano wao na watu binafsi, familia, na watoa huduma za afya kote nchini.

"Upatikanaji wa huduma kwa wakati unaofaa husababisha utambuzi wa mapema, matibabu rahisi, na matokeo bora zaidi. Bima ya afya ina jukumu muhimu katika kupunguza kutokuwa na uhakika wa kifedha na kuwawezesha watu kutafuta huduma kabla hali hazijazidi kuwa mbaya.

Mwaka unapoanza, kuna fursa ya kukabiliana na afya kwa makusudi zaidi. Kupanga mapema kupitia mpango wa afya uliopangwa si tu kuhusu kusimamia gharama za matibabu.

" Ni kuhusu kulinda ustawi, kulinda utulivu wa kifedha, na kuhakikisha mwendelezo wa huduma," anaeleza Dk. Harold Adamson

Pia anasema thamani halisi ya bima ya afya iko katika kuzuia na kuingilia kati mapema. Huduma inapotolewa kwa wakati, gharama hudhibitiwa, matokeo huboreka, na watu binafsi hubaki hai na wenye afya bora.

Hivyo anasema katika mwaka mpya, kuweka kipaumbele upangaji wa afya kunaweza kuwa mojawapo ya uwekezaji wenye maana zaidi wanaoufanya.
Ofisa Mkuu Mtendaji , Jubilee Health Insurance Dk.Harold Adamson

Mkurugenzi Mkuu wa PDPC, Dkt. Emmanuel Mkilia, akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo Januari 21, 2026 wakati wa kuzikumbusha taasisi binafsi na za umma zinazochakata taarifa binafsi kujisajili Katika tume ya Ulinzi wa Taarifa binafsi (PDPC).

Na Avila Kakingo, Michuzi Tv
TUME  ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi (PDPC) imetoa tahadhari kwa taasisi zote za umma na binafsi zinazokusanya au kuchakata taarifa binafsi kwamba hatua kali za kisheria zitaanza kuchukuliwa mara baada ya kumalizika kwa kipindi cha miezi mitatu ya nyongeza ya kujisajili.

Tahadhari hiyo inafuatia uamuzi wa Serikali wa kutoa muda wa nyongeza kuanzia Januari 8, 2026 hadi Aprili 8, 2026, kwa taasisi ambazo bado hazijazingatia matakwa ya Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi, Sura ya 44, kwa mujibu wa maelekezo ya Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mheshimiwa Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki (Mb.).

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo Januari 22, 2026, Mkurugenzi Mkuu wa PDPC, Dkt. Emmanuel Mkilia, amesema kipindi hicho ni cha mwisho cha hiari kabla ya kuanza utekelezaji mkali wa Sheria kwa taasisi zitakazokaidi.

Ameeleza kuwa baada ya Aprili 8, 2026, PDPC itaanza mara moja kufanya ukaguzi wa uzingatiaji wa Sheria kwa taasisi zote za umma na binafsi zinazokusanya, kuhifadhi, kuchakata au kusafirisha taarifa binafsi ndani na nje ya nchi.

Dkt. Mkilia amesema ukaguzi huo utalenga kubaini taasisi zitakazobainika kuendesha shughuli hizo bila usajili au kinyume na masharti ya Sheria na Kanuni zake, hatua itakayofungua mlango wa kuchukuliwa kwa hatua za kisheria.

Kwa mujibu wa PDPC, adhabu kwa watakaokiuka Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi ni pamoja na kutozwa faini, kifungo au adhabu zote kwa pamoja, sambamba na ulazima wa kulipa fidia kwa waathirika wa ukiukwaji wa haki ya faragha.

Tume imefafanua kuwa kuvunja faragha au kutumia taarifa binafsi bila ridhaa ya mhusika ni kosa linalomuwajibisha mhusika binafsi bila kujali hadhi, ukubwa au aina ya taasisi husika.

Katika wito wake, PDPC imezitaka taasisi zote za umma na binafsi kutumia ipasavyo kipindi cha miezi mitatu kilichotolewa ili kujisajili, kuimarisha mifumo ya ulinzi wa taarifa binafsi na kuepuka hatua za kisheria zitakazoanza kuchukuliwa mara baada ya muda huo kumalizika.

Sambamba na hilo, PDPC imetangaza kushiriki katika maadhimisho ya Wiki ya Faragha na Ulinzi wa Taarifa Binafsi kwa mwaka 2026 kuanzia Januari 26 hadi 30, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuongeza uelewa wa umma kuhusu haki ya faragha na wajibu wa taasisi katika kulinda taarifa binafsi.

PDPC imesisitiza itaendelea kutekeleza majukumu yake kwa uadilifu na weledi kwa lengo la kulinda taarifa binafsi za Watanzania na kuhakikisha matumizi salama ya teknolojia na huduma za kidijitali nchini.



Farida Mangube, Morogoro

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa, amewaondoa wasiwasi wanafunzi wanaosoma sayansi ya wanyama, viumbe maji na nyanda za malisho kwa kuwahakikishia kuwa hawatapoteza chochote kutokana na masomo yao, kwani sekta ya Mifugo na Uvuvi ina fursa nyingi za ajira na biashara.

Balozi Dkt. Bashiru ametoa kauli hiyo alipokutana na wanafunzi wa shahada ya kwanza wa nyanda za malisho waliokuwa kwenye mafunzo kwa vitendo ya upandaji wa malisho ya mifugo katika shamba darasa la Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA), wakati wa ziara yake ya siku moja chuoni hapo.

Katika ziara hiyo, Waziri pia alipata fursa ya kuzungumza na wataalamu wa SUA pamoja na wakurugenzi wa taasisi za Mifugo na Uvuvi zilizo chini ya Wizara yake.

Amesema kuwa bila uwepo wa malisho bora haiwezekani kufuga kwa tija, hasa kutokana na mabadiliko ya tabianchi yanayolazimisha kuwekwa mkazo mkubwa kwenye uzalishaji wa malisho.

Alieleza kuwa nyasi za asili katika nyanda za malisho zimeanza kupoteza sifa kutokana na ukame wa muda mrefu, hali iliyosababisha wafugaji wengi kupoteza mifugo yao.

“Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine ni miongoni mwa vyuo vyenye heshima kubwa nchini katika mafunzo, ushauri wa kitaalamu na utafiti kwenye kilimo, mifugo, uvuvi na misitu.” alisema Waziri.

Ameongeza kuwa Wizara yake imepewa maelekezo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050, ambayo inaelekeza kuachana na ufugaji wa kienyeji na kuelekea ufugaji wa kisasa wenye tija na ufanisi.

Aliwahimiza wanafunzi kutumia vyema elimu wanayoipata kwa kufanya tafiti zitakazowasaidia kuingia sokoni na kujiajiri, akisisitiza kuwa sekta ya malisho ni biashara kubwa na wale waliothubutu wameanza kufanikiwa.

“Msidhani mnapoteza muda. Eneo la malisho sasa ni biashara kubwa. Kuna biashara ya mbegu za malisho, uzalishaji wa malisho yenyewe na usindikaji wake ili kuyaongezea thamani. Nawapongezeni kwa kuchagua kusoma fani hii muhimu,” alisema.

Waziri alisema Wizara imekubaliana na uongozi wa SUA kuunda kamati ya pamoja itakayojumuisha Wizara na Chuo hicho, itakayosimamiwa na ofisi yake kwa kushirikiana na SUA, kwa lengo la kuimarisha tafiti, mafunzo na ushauri wa kitaalamu, hususan katika ufugaji wa samaki kwa njia ya vizimba, mabwawa, uzalishaji wa malisho na matumizi ya maabara.

“Nimetembelea maabara na nimejionea kuwa ni za kisasa na zina viwango vya kimataifa,” aliongeza.

Akizungumza na watendaji wa Wizara pamoja na menejimenti ya SUA, Dkt. Bashiru alisema bado kuna ufa mkubwa wa kimahusiano na kiutendaji kati ya Wizara na taasisi zake, na kusisitiza kuwa njia pekee ya kuuziba ni kupitia ushirikiano wa karibu.

Alisema mchango wa sekta ya Mifugo na Uvuvi katika uchumi wa taifa bado hauridhishi ikilinganishwa na rasilimali zilizopo. Alibainisha kuwa sekta ya mifugo ina mchango mzuri, lakini sekta ya uvuvi bado ina mchango mdogo licha ya Tanzania kuwa na rasilimali nyingi za uvuvi ukilinganisha na nchi nyingi za Afrika Mashariki.

Kwa upande wake, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha SUA, Profesa Raphael Chibunda, alisema kuwa licha ya changamoto ya bajeti, chuo kimekuwa kikitenga shilingi bilioni 1 kila mwaka kwa ajili ya utafiti, hususani kujenga uwezo wa watafiti wapya, kutokana na ushindani mkubwa wa kupata fedha za tafiti.

Alisema mpango huo umezaa matunda na kuiomba Wizara pamoja na taasisi zake kuweka utaratibu wa kutenga fedha mahsusi kwa ajili ya kuendeleza utafiti, hususan kwa watafiti chipukizi.







Maelfu ya wananchi wa Ikungi Mashariki katika eneo la Puma wakiwa wamekusanyika kwa wingi kwa ajili ya kumpokea, kusikiliza,kueleza kero na changamoto zao kwa Katibu wa NEC Itikadi Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi CCM Kenani Kihongosi kabla ya kuzungumza nao katika mkutano mkubwa wa hadhara,ikiwa leo ni hitimisho la ziara yake ya siku tano Mkoani Singida.













Top News