-Asema lengo ni kujenga Taifa lenye hofu ya Mungu, upendo, haki na uwajibikaji

 

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Januari 18, 2026 ameshiriki Ibada ya Jumapili katika Kanisa Kuu Anglikana la Roho Mtakatifu Dodoma na amesisitiza kwamba Serikali itaendelea kushirikiana na viongozi wa dini kujenga Taifa lenye hofu ya Mungu, upendo, haki na uwajibikaji.

“Sote tunatambua kwamba Taasisi za dini zina nafasi ya kipekee ya kuhubiri na kufundisha maadili ya upendo, uvumilivu na kuheshimiana, ambazo ni nguzo kuu za amani ya Taifa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anatambua na kuthamini sana mchango mkubwa wa taasisi za dini ikiwemo Kanisa la Anglikana, katika kudumisha amani, maadili mema na mshikamano wa Kitaifa.

 Pia, Waziri Mkuu amesema kuwa ibada za Jumapili ni sehemu muhimu ya maisha ya Mkristo na ni muda wa kujitathmini, kuimarisha mahusiano yao na Mwenyezi Mungu, na kujifunza namna bora ya kuishi kwa mujibu wa mapenzi ya Mwenyezi Mungu katika familia, jamii na Taifa kwa ujumla.

 Amesema Watanzania wanakumbushwa kuishi kwa misingi ya upendo, unyenyekevu, haki na uwajibikaji kwani Biblia inasisitiza wazi kuwa “Umejulishwa, ee mwanadamu, yaliyo mema; na Bwana anataka nini kwako, ila kutenda haki, kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu mbele za Mungu wako” (Mika 6:8) na maadili hayo si ya kidini pekee, bali ni msingi muhimu wa ustawi wa jamii na maendeleo ya Taifa.

 Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amesema Tanzania imeendelea kuwa kielelezo cha amani, umoja na mshikamano katika ukanda wetu na barani Afrika. “Amani hii si jambo la bahati, bali ni matokeo ya jitihada za pamoja za Serikali, taasisi za dini, familia na wananchi kwa ujumla.”

 Waziri Mkuu amesisitiza kuwa imani wanayojifunza na kuimarisha katika ibada inapaswa kutafsiriwa katika matendo ya uadilifu, uwajibikaji, bidii katika kazi, kuheshimu sheria na kushiriki kikamilifu katika kujenga Taifa lenye haki, amani na maendeleo endelevu. “Imani ya kweli inapaswa kuonekana kwa matendo.”

Kadhalika, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu ametumia fursa hiyo kutoa wito kwa waumini wote na Watanzania kwa ujumla kuendelea kuwa mabalozi wa amani katika familia zao, maeneo ya kazi na katika jamii kwa ujumla kupinga vitendo vyovyote vya chuki, migawanyiko na vurugu.

 Awali, Askofu wa Kanisa Anglikana Tanzania, Dayosisi ya Central Tanganyika, Dk. Dickson Chilongani ameipongeza Serikali kwa kuendelea kushirikiana na taasisi za kidini likiwemo Kanisa Anglikana na kwamba wapo pamoja na nayo katika kuhakikisha nchi inaendelea kuwa na amani. “Tunataka nchi iwe na amani ili shughuli ziendelee na hatutachezea amani.








📍Wiki ya Huduma za fedha Kitaifa kuanza viwanja vya Usagara Tanga



Na MASHAKA MHANDO, Tanga

Wizara ya Fedha imetangaza rasmi kuanza kwa maadhimisho ya Wiki ya Huduma za Fedha Kitaifa mkoani Tanga, yenye lengo la kuwajengea wananchi uwezo wa kusimamia uchumi wao na kuongeza uelewa wa masuala ya fedha nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari mkoani hapa leo, Kaimu Kamishina wa Idara ya Uendelezaji wa sekta za fedha wa Wizara ya Fedha, Dionesia Mjema msemaji ameeleza kuwa maadhimisho hayo yatafanyika katika Viwanja vya Usagara kuanzia Januari 19 hadi Januari 26, 2026.

Tukio hilo linatarajiwa kuzinduliwa rasmi na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb).

Alisema malengo ya Serikali kwa maadhimisho haya ni sehemu ya utekelezaji wa Mpango Mkuu wa Maendeleo ya Sekta ya Fedha (2020/21 – 2029/30).

Alisema serikali ya Awamu ya Sita, chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, imedhamiria kuhakikisha ifikapo mwaka 2025, asilimia 80 ya Watanzania wanakuwa na uelewa wa masuala ya fedha.

"Utafiti wa FinScope wa mwaka 2023 ulionyesha kuwa ni asilimia 53.5 tu ya nguvu kazi ndiyo inayotumia huduma rasmi za fedha. Tunataka kuwafikia wale ambao bado hawajafaidika na huduma hizi ili waboreshe maisha yao na kukuza Pato la Taifa," alisema Mjema.




Nini Kitatokea Usagara?

Chini ya kauli mbiu isemayo "ELIMU YA FEDHA, MSINGI WA MAENDELEO YA KIUCHUMI," wananchi watakaofika viwanjani hapo watapata elimu ya bure kuhusu Usimamizi wa fedha binafsi na uwekaji akiba.

Pia watajifunza utaratibu wa kukopa na kulipa madeni,Elimu ya kodi, bima, na bima ya amana,Uwekezaji katika hatifungani na masoko ya mitaji na Ulinzi wa mtumiaji wa huduma za fedha.

Alisema washiriki na Walengwa wa tukio hilo lilobeba mwavuli mpana wa wadau, likijumuisha Wizara mbalimbali kutoka Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Benki, Taasisi za bima, na asasi za kiraia.

Walengwa wakuu ni pamoja na wajasiriamali wadogo na wa kati (SMEs), wanawake, vijana, watu wenye mahitaji maalumu, wanafunzi, na watumishi wa umma.

Alisema mbinu mbalimbali kama semina, maonesho ya bidhaa, na majukwaa ya kidigitali zitatumika kufikisha ujumbe kwa wananchi watakaofika kwenye viwanja vya Usagara Jijini Tanga.

Alisema Wizara ya Fedha inatoa wito kwa wakazi wa Tanga na mikoa ya jirani kujitokeza kwa wingi kupata maarifa hayo ambayo yatatolewa na wataalamu wabobezi bila malipo yoyote.

"Hii ni fursa ya kipekee kwa mjasiriamali na mwananchi mmoja mmoja kuunganishwa na fursa za sekta ya fedha ili kukuza biashara na kuimarisha uchumi wa kaya," alisema.






WAZIRI wa Maji, Jumaa Aweso, amemuagiza Katibu Mkuu wa Wizara hiyo kufanya tathmini ya kina ya watendaji ndani ya wizara na taasisi zake na kuwaondoa wale wote "wanaohudhuria" kazini bila kuleta matokeo chanya ya wananchi kunywa maji.

Waziri Aweso alitoa kauli hiyo jana wilayani Mkinga wakati wa hafla ya kukagua na kupokea vifaa vya mabomba yenye thamani ya shilingi Bilioni 7.7, kwa ajili ya umaliziaji wa mradi wa maji wa Mkinga-Horohoro ambao sasa umefikia asilimia 65 ya utekelezaji wake.

Akizungumza kwa msisitizo, Waziri Aweso alisema tangu kuteuliwa kwake tena kuongoza wizara hiyo, amekuwa haridhishwi na namna baadhi ya watendaji wanavyotekeleza majukumu yao, akibainisha kuwa wizara inahitaji watendaji wanaopambana kukamilisha miradi na si wale wanaokwamisha huduma.

"Wizara ya maji hatutaki watu wanaohudhuria kazini, tunataka watendaji wanaoleta matokeo. Unakuwa mtendaji miaka mitano hujaenda hata kuzindua kisima kimoja? Haiwezekani. Lazima watendaji mkae mkijua kuwa wananchi wanajenga chuki na Serikali yao kwa sababu ya watumishi wasiotekeleza wajibu wao," alionya Waziri Aweso.

Aliongeza kuwa faraja ya mhandisi yeyote wa maji ni kuona wananchi wanapata huduma, na endapo hilo halifanyiki inaleta ukakasi kwa Wizara na Serikali kwa ujumla.

Katika hatua nyingine, Aweso amemtaka Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Mhandisi Mwajuma Waziri, kuhakikisha miradi viporo takribani 1,000 iliyoanzishwa nchini inakamilika haraka. Alitolea mfano wilaya ya Mkinga pekee ambayo ina miradi mitano inayohitaji kukamilishwa.

"Katibu Mkuu, nenda kafanye tathmini... wale wanaohudhuria kazini bila kufanya kazi tuwaondoe. Kama tumeweza kumaliza mradi mgumu wa Same-Mwanga, kwanini miradi mingine isua-sue? Twendeni tukafanye kazi, nami nipo tayari unipangie ziara ya kuzindua miradi na si kukagua mabomba pekee," alisisitiza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Tanga UWASA, Mhandisi Geofray Hilly, alibainisha kuwa mradi huo wa Mkinga-Horohoro wenye thamani ya shilingi Bilioni 35, unakwenda kunufaisha wananchi 57,000 waliopo katika vijiji 37.

Katibu Mkuu, Mhandisi Mwajuma Waziri, alimhakikishia Waziri kuwa ameshamuelekeza mkandarasi kuongeza nguvu kazi ili mradi huo ukamilike ifikapo Julai mwaka huu, huku Mbunge wa Jimbo la Mkinga, Twaha Mwakioja, akishukuru kwa hatua hiyo akisema ni mkombozi dhidi ya adha ya kufuata maji umbali mrefu.

Waziri Aweso alihitimisha kwa kusema kuwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amekuwa akitoa fedha nyingi katika sekta ya maji, hivyo ni wajibu wa watendaji kuunga mkono juhudi hizo kwa uadilifu na kasi ya matokeo.








Katibu wa NEC Itikadi uenezi na mafunzo CCM, Ndugu Kenani Labani Kihongosi, ametembelea na kukagua ujenzi na ukarabati wa Hospitali ya Wilaya ya Manyoni, mradi uliokamilika kwa asilimia 100 kwa gharama ya Shilingi bilioni 1.4.

Hospitali hiyo ina majengo yote muhimu pamoja na vifaa vya kisasa vya tiba, vinavyoboresh­a huduma za afya kwa wananchi wa Manyoni na maeneo ya jirani, hususan katika kupunguza vifo vya mama na mtoto na kuongeza ufanisi wa huduma za afya.

Akizungumza baada ya ukaguzi, Ndugu Kihongosi alitoa pongezi za dhati kwa Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuelekeza fedha nyingi katika sekta ya afya, akisisitiza kuwa huo ni ushahidi wa uongozi unaoweka mbele maslahi ya wananchi.

Aidha, aliwapongeza wananchi wa Manyoni kwa ushiriki wao katika shughuli za maendeleo, akieleza kuwa mchango wa wananchi ni nguzo muhimu ya maendeleo ya Taifa. Vilevile aliipongeza Serikali kwa usimamizi mzuri na uwajibikaji wa mradi huo uliogharimu fedha nyingi za umma.

Ndugu Kihongosi aliwataka Watanzania kutembea na kujionea kwa vitendo kasi ya maendeleo inayopatikana chini ya Serikali ya CCM, akisisitiza kuwa CCM ni Chama cha vitendo, matokeo na maendeleo ya kweli.









Na OWM - TAMISEMI 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amemuelekeza Mkandarasi MCB Company LTD, Mbeya University of Science and Technology kukamilisha ujenzi wa Jengo la Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro ifikapo Julai 2026.

Prof. Shemdoe ametoa maelekezo hayo Januari 17, 2026 mjini Morogoro, wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua  miradi ya maendeleo  ambapo alianza ukaguzi  wa mradi huo wa Jengo la Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro,  ambao ulianza kutekelezwa rasmi Mei 27, 2022 na ulitakiwa kukamilika Mei 26, 2024.

“Ninaelekeza mwezi Julai jengo liwe limekamilika, kwani fedha ipo, Mshauri Elekezi ambaye ni Wakala wa Majengo upo na Mkandarasi upo,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Sanjari na hilo, amemtaka Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Malima kutomuongezea muda mkandarasi iwapo atashindwa kukamilisha ujenzi wa jengo hilo, na kuelekeza atafutwe mkandarasi mwingine atakayekamilisha jengo hilo kwa wakati.

Prof. Shemdoe amemuhimiza Mshauri Elekezi TBA kuhakikisha anatekeleza wajibu wake kikamilifu na kuahidi kurejea mwezi Julai ili kujiridhisha iwapo maelekezo yake yametekelezwa, na kuongeza kuwa mwaka 2022 alishuhudia ujenzi wa msingi wa jengo hilo  la Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro akiwa ni Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais-TAMISEMI. 

Aidha, amemtaka Mshitiri ambaye ni Katibu Tawala wa Mkoa wa Morogoro Dkt. Mussa Ali Mussa kukutana na Mshauri Elekezi TBA pamoja na Mkandarasi MCB Company Limited ili kuandaa mpango kazi wa kukamilisha ujenzi wa jengo hilo na kuuwasilisha kwake ndani ya wiki moja.

Kwa upande wake, Msanifu Majengo Bw. Justine Katabaro kutoka kampuni ya MCB Company Ltd iliyopewa kandarasi amesema kuwa wamepokea maelekezo ya Prof. Shemdoe ya kukutana na mshitiri pamoja mshauri elekezi ili kuandaa mpango kazi utakaowezesha kukamilisha ujenzi wa jengo la Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Morogoro na kulikabidhi mwezi Julai, 2026.

Awali akitoa taarifa ya ujenzi, Mhandisi Khamadu Kitunzi kutoka TBA amesema jengo hilo ni la ghorofa  tatu (3), ambapo sakafu ya chini imetengwa kwa ajili ya maegesho ya magari ya watu mashuhuri na ofisi ya madereva na sakafu ya kwanza na ya pili imetengwa kwa ajili ya ofisi za watumishi na ukumbi huku sakafu ya tatu ikitengwa kwa ajili ya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa na Ofisi ya Katibu Tawala wa Mkoa.





 

Katibu wa NEC Itikadi Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Komredi Kenani Labani Kihongosi,ametembelea Shina Namba 7 la CCM katika Tawi la Manyoni Mjini, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kimkakati ya kuimarisha uhai wa Chama kuanzia ngazi ya mashina mkoani Singida.

Akiwa katika shina hilo lenye wanachama 150, Ndugu Kihongosi aliwashukuru wanachama na uongozi wa Shina Namba 7 kwa mshikamano, nidhamu na uongozi wao thabiti. Alisisitiza kuwa huo ndiyo utofauti wa CCM na vyama vingine, kwa kuzingatia muundo imara wa Chama, Katiba yake na uongozi madhubuti kuanzia ngazi ya taifa hadi mashinani.

Aidha, aliwasilisha salamu za Mwenyekiti wa CCM ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, na kueleza kuwa hata yeye ameendelea kujifunza misingi ya uongozi bora kutoka kwa viongozi wa mashina, akitaja Shina Namba 7 kama mfano wa uongozi wa karibu na wananchi.

Amewahakikishia wananchi na wanachama wa shina hilo kuwa CCM itaendelea kuleta maendeleo.

Kazi na Utu tunasongambele.












Na Mwandishi wetu, Babati


MBUNGE wa Jimbo la Babati Mjini, Mkoani Manyara, Emmanuel Khambay amewataka maofisa ardhi wa Halmashauri ya Mji huo kufanya kliniki ya ardhi kwenye kata ili kuondoa migogoro ya ardhi inayowakabili baadhi ya wananchi.

Khambay ametoa agizo hilo kwenye kata ya Maisaka katika ziara ya kushukuru kwa kuchaguliwa na kusikiliza kero, malalamiko na changamoto zinazowakabili wakazi wa eneo hilo.

Ameeleza kwamba miongoni mwa malalamiko, kero na changamoto alizozipata katika jamii ni migogoro ya ardhi kwenye kata ya Maisaka hivyo maofisa ardhi waanzishe kliniki katika eeo hilo.

"Maofisa ardhi wa halmashauri anzisheni kliniki ya ardhi na kukutana na wakazi wa kata ya Maisaka, msikilize changamoto zao na kuwapatia majawabu," amesema Khambay.

"Lengo la ziara hii ni kuwashukuru na kusema asante kwa kunichagua na kusikiliza kero mbalimbali na miongoni mwa changamoto nilizozisikia ni migogoro ya ardhi," amesema Khambay.

Amesema tiba ya migogoro ya ardhi ni kuanzisha kliniki ya ardhi kwa maofisa ardhi kutoka ofisini na kwenda kwa watu kusikiliza matatizo yao na kueleza namna ya kuyatatua.

Hata hivyo, amewaahidi wakazi wa eneo hilo, kuendelea kushirikiana nao kufanikisha maendeleo na kutoa huduma bora bila upendeleo wowote ule.

Mwenyekiti wa CCM wa wilaya ya Babati mjini, Elizabeth Malley amempongeza Khambay kwa kushika nafasi hiyo na kujitoa kwa ajili ya kuwatumikia wananchi wa mjini Babati.

Malley anewaomba wakazi wa Babati mjini wampe ushirikiano wa kutosha mbunge wao ili aweze kuwatumikia ipasavyo kwani uchaguzi umeshafanyika na kilichobaki ni kufanyika maendeleo.

Mmoja kati ya wakazi wa kata ya Maisaka, Rose John amepongeza hatua hiyo ya kufanyika kwa kliniki ya ardhi itakayofanywa na maofisa ardhi wa halmashauri hiyo.

Amesema kupitia kliniki hiyo itakayofanywa wataweza kumaliza migogoro ya ardhi ambayo kwa namna moja au nyingine inazorotesha maendeleo.



Manyoni, Singida, Januari 18, 2026

Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Kenani Labani Kihongosi, ameanza rasmi ziara yake ya kimkakati leo tarehe 18 Januari 2026 mkoani Singida, ambapo ameanzia Wilaya ya Manyoni.

Ziara hii ni ziara maalum ya Chama Cha Mapinduzi inayolenga kuhakikisha Chama kinawafikia wanachama wote nchini sambamba na kusikiliza kero za wananchi, kuzifanyia kazi na kuhakikisha zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati.

Akizungumza na wanachama walio jitokeza, Ndugu Kihongosi aliwasilisha salamu za Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan. Alisisitiza umuhimu wa umoja, mshikamano na upendo.






Ubalozi wa Tanzania nchini Sweden umeratibu na kushiriki katika Maonesho ya Kimataifa ya Utalii ya Matka yanayofanyika jijini Helsinki, Finland, kuanzia tarehe 14-18 Januari, 2026, huku ukitangaza vivutio vya utalii vya Tanzania pamoja na filamu ya Tanzania: The Royal Tour.

Maonesho hayo ni miongoni mwa maonesho makubwa barani Ulaya yakijumuisha kampuni 950 za utalii, usafiri wa ndege, vyombo vya habari, na ushauri elekezi wa utalii kutoka duniani kote ambapo katika siku ya kwanza yalipokea washiriki 56,000 wakiwemo watalii watarajiwa.

Kampuni binafsi za Lifestyle Safaris & Holidays na Lifetime Safaris za Tanzania nazo zinashiriki katika maonesho hayo zikiwa na timu ya Ubalozi wa Tanzania. Nchi zingine za Afrika zinazoshiriki ni Uganda, Kenya, Ushelisheli, Namibia, Afrika Kusini, Senegal, Moroko, Tunisia na Misri.

Balozi wa Tanzania nchini Sweden, Mhe. Mobhare Matinyi, anayeiwakilishia pia Tanzania katika nchi za Nodiki, Baltiki na Ukraina, alitumia jukwaa kuelezea namna Tanzania ilivyopata heshima kubwa ya kushinda Tuzo za Utalii za Dunia tarehe 6 Desemba 2025, nchini Bahrain, ikiwa ni mwaka wa tatu mfululizo.

Balozi Matinyi alielezea pia namna Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, alivyoshiriki na kuigiza katika filamu ya kuitangaza Tanzania ya dakika 57 iitwayo Tanzania: The Royal Tour akiwa na mwandishi wa Marekani mshindi wa Tuzo ya Emmy, Peter Greenberg, mwaka 2022.

Balozi Matinyi aliiambia hadhira kwamba Tanzania ina vivutio vitatu kati ya Maajabu Saba ya Asili ya Afrika na pia maeneo saba yanayotambuliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) kama Urithi wa Dunia, akiutaja mathalani Mlima Kilimanjaro, uhamaji mkubwa wa wanyamapori hifadhini Serengeti na bonde la Ngorongoro. Mbali ya hifadhi za taifa 22, Balozi Matinyi pia alitaja utajiri wa utamaduni wa makabila 126 ya Tanzania, hifadhi za historia ya kale kama michoro ya mapangoni ya Kondoa, Mji Mkongwe wa Zanzibar na miji ya Bagamoyo na Kilwa.

Balozi Matinyi pia alitumia maonesho hayo kufanya mazungumzo na wadau mbalimbali wakiwemo Afisa Mtendaji Mkuu wa Atlantic Link, Bi. Karin Gert Nielsen na Mwakilishi wa Danish Travel Show, zote za Denmark, Bw. Johnny Frandsen; Meneja wa kampuni ya Flygresor ya Sweden, Bw. Peter Hallgren; na kwa kampuni za Finland Mwanzilishi na Mkurugenzi Mwendeshaji wa GapEdu, Bw. Jyrki Nilson; Mkurugenzi Mwendeshaji wa Amanihoiva Limited, Bw. Juha Valtanen na Mwakilishi wa Matka Travel Fair, Inkeri Vainik. Mazungumzo hayo yalilenga namna ya kushirikiana katika kuutangaza zaidi utalii wa Tanzania barani Ulaya.


Imetolewa na:
Ubalozi wa Tanzani nchini Sweden,
17 Januari, 2025.








Na Oscar Assenga, MKINGA

WAZIRI wa Maji Jumaa Aweso amemtaka Mkandarasi anayetekeleza mradi wa Maji Mkinga – Horohoro kuhakikisha wanafanya kazi usiku na mchana kuukamilisha kwa wakati ili wananchi waweze kupata huduma ya maji safi na salama.

Aweso aliyasema hayo leo wakati wa halfa ya Mapokezi ya Vitendea kazi (Mabomba) vitakavyotumika katika utekelezaji wa Mradi wa Maji Mkinga-Horohoro ambao unagharimu kiasi cha Bilioni 35.



Halfa hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi Tanga Uwasa,Dkt Ally Fungo,Mkurugenzi wa Tanga Uwasa Mhandisi Geofrey Hilly,Meneja wa Ruwasa Mkoa wa Tanga Mhandisi Upendo Lugongo pamoja na watumishi wa Tanga Uwasa,Ruwasa,Viongozi wa CCM na wananchi wa eneo la Manza.

Alisema kutokana na kwamba mradi huo ni muhimu kwa wananchi ambao wanakabiliwa na changamoto ya maji hivyo wahakikishe unakamalika kwa wakati na ujenzi wake uwe tofauti uende na maji katika maeneo yanayolazwa mabomba nao wapate maji.



“Tunajua tuna miradi mingi sana lakini nikuombe Katibu Mkuu utoe fedha ili mradi huo ukamilike kwa wakati ili wana Mkinga waweze kupata huduma ya maji safi na salama”Alisema



“Kama mnakumbuka tulimleta Rais Dkt Samia Suluhu aliweke kuweka jiwe la msingi kukamilika kwake tumuombe Rais aje kuzindua mradi huu wa Mkinga sababu ndio muasisi na ndio aliyweka jiwe la msingi”Alisema

Waziri Aweso aliwataka wafanye kazi hiyo kwa uadilifu na uaminifu ili kuhakikisha hiyo kazi inakamilika na wana Mkinga waweze kupata maji safi na salama



Hata hivyo Waziri huyo alimuahidi Mbunge wa Jimbo la Mkinga Twaha Mwakiojakwamba watafanya kazi kuhakikisha wanakamilisha mradi huo kutokana na kwamba wapo baadhi ya watumishi wanaishi Tanga kutokana na changamoto ya maji wakikamilisha mradi huo watapata maendeleo makubwa.


Alisema maendeleo hayo yatapatikana kwa wana Mkinga na wawekezaji mbalimbali watakwenda kuwekeza hiyo kazi wameibeba na kufanya kazi usiku na mchana ili kuhakikisha mradi unakamilika.


Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Gilbert Kailima alisema wanaishukuru Serikali kutokana na kwamba mradi huo ni mkombozi mkubwa kwa wananchi wa wilaya ya Mkinga na utaondoa adha kubwa ya Maji.


Alisema wanamshukuru Rais kwa kutoa kipaumbele sana katika mradi huo na ndio maana alikuja kuweka jiwe la Msingi katika mradi huo na kuhaidi watajitahidi kusimamia mradi huo kwa karibu kwa kushirikiana na Tanga Uwasa ili utekelezwe kwa wakati ili uanze kufanya kazi kama Rais anavyotamani iwe pamoja nawe.

Aidha alisema katika wilaya hiyo wana miradi mengine mikubwa iliyopo wilayani humo ikiwemo wa Gombero, Mapatano, Muhinduro na Bamba Mwarongo yote ni mikubwa ambayo Serikali chini ya Wizara ya Maji inaendelea kutenga fedha kwa ajili ya utekelezaji wake na ipo katika hatua mbalimbali.


“Kutokana na kwamba umefika leo tunaomba nayo hii miradi waone namna gani inaweza kuisha kwa wakati kama ambavyo wananchi wa Mkinga wanatamani iwe tunaimani sana na utendaji wako na katibu mkuu wa wizara ya Maji “Alisema.


Alitoa wito kwa wananchi wa wilaya hiyo kutoa ushirikiano kwa mkaandarasi ambaye atatoa huduma ya usambazaji wa maji katika mradi huo na kuhakikisha vifaa vyake havihujumiwi badala yake wawe walinzi ili kufanya kazi yake vizuri.

Naye kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Mkinga (CCM) Twaha Mwakioja alisema kwamba katika taifiti iliyofanywa changamoto kubnwa inawakabili zaidi ya wananchi asilimia 80 wamelalamikia hali ya upatikanaji wa maji.



Alisema kwamba mradi huo kabla ya kuanza kutekelezwa wastani wa upatikanaji wa maji katika wilaya ya Mkinga ni asilimia 60 mpaka 69 hivyo wana imani mradi huo utakapokamilika upatinaji wa maji utafika zaidi ya asilimia 88 mradi huo ni mkombozi mkubwa kwao.

Aidha alisema kwamba mradi huo utakakamilika zaidi ya vijiji 37 vinakwenda kupata maji safi na salama ya uhakika na Serikali imeweka fedha nyingi ili kuhakikisha unakamilika ili wananchi waweze kuondokana na adha ya maji.

“Mhe Waziri tunaomba mradi huu kwa maana umesuasua kwa mude mrefu kama unavyotambua upo nyuma zaidi ya miaka miwili na ifikapo julai mradi uwe umekamilika hivyo tunashukuru na wananchi wana mategemeo makubwa sana “Alisema

Mwisho

Top News