Arusha, Tanzania, Juni 27, 2026 – Maadhimisho ya Siku ya Bima yamehitimishwa kwa mafanikio kupitia mashindano ya gofu ya ICEA LION King of the Course, yaliyowakutanisha wataalamu wa sekta ya bima, viongozi wa biashara na wadau mbalimbali kwa siku ya ushindani, kujenga mahusiano na kubadilishana uzoefu.

Mashindano hayo, yaliyodhaminiwa na ICEA LION General Insurance, yalidhihirisha dhamira ya kampuni hiyo ya kuendelea kuunga mkono mipango inayokuza ushirikiano ndani ya sekta ya bima huku yakihamasisha ushindani wenye tija na kuimarisha mahusiano ya kitaaluma.

Karim Jamal aliibuka mshindi wa jumla na kutwaa taji la King of the Course (Mfalme wa Uwanja). Kutokana na ushindi huo, amejishindia safari yenye udhamini kamili ya kuiwakilisha Tanzania katika fainali za King of the Course, zitakazofanyika Mombasa, Kenya, mwezi Oktoba mwaka huu. Aidha, alikabidhiwa zawadi mbalimbali wakati wa hafla ya utoaji wa tuzo.

Mashindano hayo yalihudhuriwa na viongozi wa ICEA LION Group, viongozi wa Taasisi ya Bima Tanzania (Insurance Institute of Tanzania – IIT) pamoja na wadau wengine kutoka sekta ya bima, wakionesha mshikamano na dhamira ya pamoja ya kuendeleza sekta hiyo nchini.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Jared Awando, Mtendaji Mkuu wa ICEA LION General Insurance Tanzania, alisema kampuni hiyo itaendelea kuunga mkono mipango inayojenga ushirikiano na kuimarisha maendeleo ya sekta ya bima.

"Katika ICEA LION tunaamini kuwa mahusiano imara ni msingi wa kujenga sekta ya bima yenye uimara na uwezo wa kukidhi mahitaji ya wateja. Tunajivunia kuunga mkono mipango inayowaleta pamoja wataalamu wa sekta hii huku tukisherehekea ubora ndani na nje ya uwanja wa gofu," alisema.

Mashindano hayo yalihitimisha rasmi maadhimisho ya Siku ya Bima mwaka huu, yakionesha dhamira ya wadau wa sekta hiyo ya kuimarisha ushirikiano, taaluma na kuongeza uelewa wa umma kuhusu umuhimu wa bima katika kukuza ustahimilivu wa kiuchumi.




Kuhusu ICEA LION General Insurance

ICEA LION General Insurance imekuwa ikitoa huduma za bima nchini Tanzania tangu mwaka 1999. Kampuni hiyo hutoa huduma mbalimbali za bima, ikiwemo bima za magari, afya, mali na biashara, kwa lengo la kuwasaidia watu binafsi na taasisi kulinda mali na shughuli zao dhidi ya hatari mbalimbali.

Ikiendeshwa chini ya ahadi yake ya chapa ya Simba wa Bima, ICEA LION imejizatiti kutoa huduma za bima zenye ubunifu na zinazotegemewa, zinazowapa wateja ujasiri wa kusonga mbele kwa kujiamini. Kama sehemu ya ICEA LION Group, mojawapo ya makundi yanayoongoza kwa huduma za kifedha Afrika Mashariki, kampuni hiyo inaendelea kuhamasisha matumizi ya bima na kuimarisha ustahimilivu wa kifedha nchini Tanzania.
Bw. Jared Awando (wa tatu kutoka kushoto), Mtendaji Mkuu wa ICEA LION General Insurance Tanzania, akiwa pamoja na washindi wa mashindano ya gofu ya ICEA LION King of the Course na viongozi wa ICEA LION Group mara baada ya hafla ya utoaji wa tuzo iliyofanyika jijini Arusha. Mashindano hayo, yaliyofanyika ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Bima, yalimshuhudia Karim Jamal akitwaa ubingwa wa jumla na kujishindia safari yenye udhamini kamili ya kuiwakilisha Tanzania katika fainali za King of the Course zitakazofanyika Mombasa, Kenya, mwezi Oktoba mwaka huu, pamoja na zawadi nyingine mbalimbali.

Na Janeth Raphael MichuziTv

Bodi ya Kitaaluma ya Ununuzi na Ugavi (PSPTB) imetangaza matokeo ya mitihani ya 33 ya taaluma ya Mnyororo wa Ugavi iliyofanyika nchini kuanzia Mei 11 hadi 15, 2026, huku jumla ya watahiniwa 682 sawa na asilimia 43.7 wakifaulu.

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dodoma, Mkurugenzi Mtendaji wa PSPTB, Godfrey Mbanyi, amesema jumla ya watahiniwa 1,632 walikuwa wamesajiliwa kufanya mitihani hiyo, lakini watahiniwa 1,559 ndio walioifanya, huku watahiniwa 73 wakishindwa kushiriki kutokana na sababu mbalimbali.

Amesema kati ya watahiniwa waliofanya mitihani hiyo, watahiniwa 682 (asilimia 43.7) wamefaulu, watahiniwa 773 (asilimia 49.6) wamepata hadhi ya referral na watarudia baadhi ya masomo yao, huku watahiniwa 104 (asilimia 6.7) wakifeli na kulazimika kuanza upya masomo katika ngazi husika.

Mbanyi amesema bodi inawahimiza watahiniwa waliopata referral na wale waliofeli kujisajili kwa ajili ya mitihani ya kati (Mid-Session Examinations) itakayofanyika Agosti 24 hadi 28, 2026, au kushiriki mitihani ya Novemba 2026 ili kuboresha matokeo yao.

Ameongeza kuwa dirisha la usajili kwa ajili ya mitihani ya kati litafunguliwa kuanzia Julai 1 hadi Agosti 7, 2026.

Aidha, aliwataka watahiniwa wenye hadhi ya Last Chance Referral kutumia ipasavyo fursa ya mitihani ya kati au ya Novemba 2026, kwani ndiyo nafasi yao ya mwisho ya kukamilisha ngazi za mitihani wanazosomea.

Katika hatua nyingine, PSPTB imewaalika watahiniwa wote wa ngazi ya CPSP II waliofaulu kushiriki warsha ya utafiti itakayofanyika mwishoni mwa Julai 2026, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya hatua zinazofuata katika taaluma yao.

Mbanyi pia ametoa wito kwa wahitimu wa vyuo vikuu vya ndani na nje ya Tanzania kujisajili kufanya mitihani ya kitaaluma ya PSPTB ili kupata sifa zinazotambulika kitaaluma katika fani ya Ununuzi na Ugavi.

Vilevile, amewataka wazazi, wadhamini na waajiri kuendelea kuwawezesha watahiniwa kwa kulipia ada za maandalizi na mitihani, akisema hatua hiyo itasaidia kuongeza idadi ya wataalamu wenye ujuzi na maarifa katika sekta ya ununuzi na ugavi.

Hata hivyo, PSPTB imesisitiza kuwa haitavumilia vitendo vya ukiukwaji wa kanuni na taratibu za mitihani. Mbanyi alisema bodi itaendelea kuchukua hatua kali za kinidhamu dhidi ya watakaobainika kufanya udanganyifu au kukiuka maadili ya mitihani.

Alieleza kuwa adhabu zinazoweza kutolewa kwa mujibu wa kanuni ni pamoja na kufutwa kwa matokeo ya mitihani, kusimamishwa kushiriki mitihani kwa kipindi cha hadi miaka mitatu, pamoja na adhabu nyingine za kisheria ikiwemo faini au kifungo cha jela kulingana na uzito wa kosa.

Kwa mujibu wa PSPTB, hatua hizo zinalenga kulinda uadilifu wa mitihani na kuhakikisha taaluma ya Ununuzi na Ugavi inaendelea kujengwa katika misingi ya maadili, weledi na uwajibikaji.


Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), kwa ufadhili wa Green Climate Fund (GCF), kwa kushirikiana na Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEP) na Taasisi ya Utafiti wa Misitu Tanzania (TAFORI), imefikia hatua muhimu katika utekelezaji wa Mradi wa Kujenga Uhimilivu dhidi ya Athari za Mabadiliko ya Tabianchi katika Mkoa wa Kigoma kwa kuanza uthibitishaji wa matokeo ya tathmini ya awali (Baseline Survey) ya mradi huo kabla ya kuanza kwa zoezi muhimu la Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi kwa vijiji 22 vilivyopo katika wilaya za Kasulu, Kakonko na Kibondo.

Uthibitishaji huo unafanyika kupitia warsha inayofanyika katika Wilaya ya Kibondo, Mkoa wa Kigoma, na unalenga kuhakiki hali halisi ya kijamii, kiuchumi na kimazingira katika maeneo ya mradi kabla ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za kuimarisha uhimilivu wa jamii dhidi ya mabadiliko ya tabianchi.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa warsha hiyo, Meneja wa Mradi kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira, Mhandisi Onesphory Kamukuru, alisema mradi unatekelezwa katika wilaya za Kasulu, Kibondo na Kakonko kutokana na maeneo hayo kuathiriwa kwa kiwango kikubwa na uharibifu wa mazingira, mmomonyoko wa ardhi na athari nyingine za mabadiliko ya tabianchi.

Alieleza kuwa mojawapo ya sababu zilizochangia uharibifu huo ni historia ya maeneo hayo kupokea idadi kubwa ya wakimbizi, hali iliyosababisha ongezeko la matumizi ya rasilimali za misitu, ikiwemo ukataji wa miti kwa ajili ya kuni na mkaa.

“Mradi huu ni wa wananchi na unatekelezwa katika maeneo matatu makuu ambayo ni kilimo mseto, usimamizi wa hifadhi za misitu ya vijiji na za TFS pamoja na kurejesha maeneo yaliyoharibiwa na mmomonyoko wa ardhi,” alisema Mhandisi Kamukuru.

Mradi huo unatekelezwa katika vijiji 22 vya wilaya za Kasulu, Kibondo na Kakonko, ambavyo vimeathiriwa kwa kiwango kikubwa na mabadiliko ya tabianchi na uharibifu wa mazingira, hususan vijiji vilivyo karibu na maeneo yaliyowahi kuhifadhi wakimbizi.

Katika mradi huu, TAFORI imepewa jukumu la kukusanya na kuchambua taarifa za awali zitakazotumika kama msingi wa ufuatiliaji na tathmini ya utekelezaji wa mradi. Aidha, taasisi hiyo inasimamia utekelezaji wa shughuli za kitaalamu katika maeneo matatu ya kipaumbele ambayo ni Usimamizi Shirikishi wa Misitu ya Jamii (CBFM), Kilimo Mseto (Agroforestry) na Upandaji Miti (Afforestation).

Akizungumza kwa niaba ya timu ya wataalamu wa TAFORI, Mtafiti Mwandamizi na Msimamizi wa Ushauri wa Kitaalamu wa Mradi, Dkt. Numan Amanzi, alisema matokeo ya tathmini ya awali yaliyowasilishwa kwa wadau yameridhisha na yanaakisi hali halisi iliyopo katika vijiji vinavyotekeleza mradi.

“Matokeo haya yatatumika kama msingi wa kupima mafanikio ya mradi baada ya kukamilika ili kubaini kwa kiwango gani umechangia kuboresha hali za kiuchumi, kijamii na kimazingira katika jamii husika,” alisema Dkt. Amanzi.

Hatua ya uthibitishaji wa matokeo ya tathmini ya awali ni awamu ya tatu ya utekelezaji wa mradi. Awamu ya kwanza ilihusisha utambulisho wa mradi kwa mamlaka za Mkoa wa Kigoma na wilaya husika, huku awamu ya pili ikihusisha uthibitishaji wa vigezo vya uteuzi wa vijiji, maeneo ya utekelezaji na aina za miti zitakazotumika katika shughuli za usimamizi shirikishi wa misitu, kilimo mseto na upandaji miti.

Warsha hiyo imewakutanisha wadau mbalimbali wakiwemo wawakilishi kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Maafisa Mazingira,  Maafisa Mkoa, Wilaya na Wakala wa Huduma za Misitu (TFS)  na Wawakilishi wa vijiji 22 vya wilaya za Kasulu, kibondo na Kakonko.



Na Mwandishi Wetu, Kondoa

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt. Leonard Akwilapo, amesema Serikali itaendelea kushirikiana kwa karibu na taasisi za kidini katika kuboresha huduma za jamii, hususan sekta za elimu, afya na malezi, kwa kutambua mchango mkubwa wa taasisi hizo katika maendeleo ya taifa.

Dkt. Akwilapo ameyasema hayo Juni 28, 2026, mkoani Dodoma aliposhiriki Harambee ya Ujenzi wa Nyumba za Walimu katika Shule ya St. Peters and St. Paul Secondary School iliyopo Wilaya ya Kondoa. Hafla hiyo ilihudhuriwa pia na Baba Askofu wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Kondoa, Askofu Given Gaula, pamoja na viongozi na waumini wa kanisa hilo.

Katika hafla hiyo, Waziri huyo alishiriki pia ibada maalumu ya kumsimika mfadhili kutoka Uingereza, Bw. Peter Ruxton, kuwa Lay Canon wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Kondoa kutokana na mchango wake mkubwa katika maendeleo ya elimu na shughuli za kanisa.

Akizungumza katika hafla hiyo, Dkt. Akwilapo alisema Serikali inaendelea kutekeleza maelekezo ya Rais ya kuimarisha ushirikiano na madhehebu mbalimbali ya dini kwa lengo la kuboresha huduma za jamii zinazowagusa wananchi moja kwa moja.

"Rais amekuwa akituambia kuwa ataendelea kushirikiana na madhehebu ya dini, na azma yake ni kuboresha huduma za jamii," alisema Dkt. Akwilapo.

Alisema Serikali inatambua mchango mkubwa wa Kanisa la Anglikana katika sekta ya elimu, akibainisha kuwa kwa mujibu wa takwimu za Wizara ya Elimu, kanisa hilo linaendesha shule za awali 39, shule za msingi 40, shule za sekondari 17, vyuo vya kati 17 pamoja na chuo kikuu kimoja.

Alieleza kuwa taasisi hizo zimeendelea kutoa mchango muhimu katika kuwajengea vijana maarifa, maadili, uzalendo na hofu ya Mungu, mambo ambayo ni msingi wa maendeleo endelevu ya taifa.

Aidha, Dkt. Akwilapo aliipongeza Dayosisi ya Kondoa kwa juhudi zake za kupanua huduma za elimu kwa kuongeza idadi ya shule, akieleza kuwa hivi karibuni shule nyingine itazinduliwa katika wilaya hiyo.

Kwa upande wake, Askofu wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Kondoa, Dkt Given Gaula, amesema ili kumtia moyo mfadhili anayesaidia maendeleo ya kanisa ikiwemo ujenzi wa shule waumini wa kanisa hilo wanapaswa kuchanga fedha kwa ajili ya maendeleo ya ujenzi wa nyumba za walimu.

‘’Shule zinazoendeshwa na kanisa la Angilikana hapa Kondoa zimeleta mabadiliko makubwa katika maisha ya watoto kwa kutoa elimu bora bila ubaguzi wa dini au itikadi’’. amesema

Jumla ya shilingi milioni tano zilichangwa katika hafla hiyo ikiwa ni jitihada za kumuunga mkono mfadhili anayejenga nyumba za walimu katika Shule za St. Peters and St. Paul Secondary School iliyopo Wilaya ya Kondoa

Katika hatua nyingine, Dkt. Akwilapo alimpongeza Bw. Peter Ruxton baada ya kusimikwa kuwa Lay Canon, akisema ametoa mchango wa kipekee katika maendeleo ya elimu na shughuli za kanisa kwa miaka mingi.

Alisema Serikali inathamini mchango wa mfadhili huyo, ambaye amesaidia kujenga na kuendeleza shule mbalimbali pamoja na kuchangia maendeleo ya taasisi za kidini zinazotoa huduma kwa jamii bila ubaguzi.

Naye Askofu Dkt Given Gaula alisema Bw. Ruxton amekuwa mshirika muhimu wa Dayosisi ya Kondoa, akibainisha kuwa karibu asilimia 97 ya shule zinazomilikiwa na dayosisi hiyo zimejengwa kwa msaada wake. 

Aidha, amesema mfadhili huyo amechangia ununuzi wa mabati kwa makanisa mengi yaliyopo vijijini na kusaidia miradi mingine ya maendeleo inayowanufaisha wananchi.

Alisisitiza kuwa ushirikiano kati ya Serikali, taasisi za kidini na wadau wa maendeleo unaendelea kuwa chachu muhimu katika kuimarisha elimu, kuboresha ustawi wa jamii na kuharakisha maendeleo ya taifa.Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt. Leonard Akwilapo akizungumza wakati wa Harambee ya Ujenzi wa Nyumba za Walimu katika Shule ya St. Peters and St. Paul Secondary School iliyopo Wilaya ya Kondoa jana.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt. Leonard Akwilapo akiendesha Harambee ya Ujenzi wa Nyumba za Walimu katika Shule ya St. Peters and St. Paul Secondary School iliyopo Wilaya ya Kondoa.Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt. Leonard Akwilapo akishiriki ibada wakati wa Harambee ya Ujenzi wa Nyumba za Walimu katika Shule ya St. Peters and St. Paul Secondary School iliyopo Wilaya ya Kondoa tarehe 28 Julai 2026.Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt. Leonard Akwilapo akipongezwa alipopatiwa zawadi mara baada ya kuendesha Harambee ya Ujenzi wa Nyumba za Walimu katika Shule ya St. Peters and St. Paul Secondary School iliyopo Wilaya ya Kondoa.

 Mfadhili kutoka Uingereza Bw. Bw. Peter Ruxton akisimikwa kuwa Lay Canon wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Kondoa kutokana na mchango wake mkubwa katika kanisa hilo jana.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt. Leonard Akwilapo akiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa Kanisa la Anglikana mara baada ya kuendesha Harambee ya Ujenzi wa Nyumba za Walimu katika Shule ya St. Peters and St. Paul Secondary School iliyopo Wilaya ya Kondoa.
Given Gaula wa Kanisa la Anglikana akiwa katika picha na viongozi wa kanisa hilo mara baada ya kumsimika Bw. Peter Bw. Peter Ruxton kuwa Lay Canon wa kanisa la Anglikana Dayosisi ya Kondoa.


Sehemu ya waumini wakiwa katika Harambee ya Ujenzi wa Nyumba za Walimu katika Shule ya St. Peters and St. Paul Secondary School iliyopo Wilaya ya Kondoa.



Dar es Salaam, Julai 2026

Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), Dkt. Ernest Mabonesho, ametangaza kuwa kilele cha maadhimisho ya miaka 25 tangu kuanzishwa kwa Chuo kitafanyika tarehe 3 Julai 2026 katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam, kuanzia saa 3:00 asubuhi.

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam, Dkt. Mabonesho amesema kuwa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kilianzishwa mwaka 2000 kwa lengo la kuimarisha utendaji, ufanisi na weledi katika utumishi wa umma nchini, na kwamba mwezi Agosti 2025 Chuo kilitimiza miaka 25 tangu kuanzishwa kwake.

Katika kuadhimisha miaka 25 ya Chuo, shughuli mbalimbali za kijamii, kitaaluma na maendeleo ya jamii zimetekelezwa katika kampasi zote sita za Chuo zilizopo Dar es Salaam, Tabora, Mtwara, Singida, Tanga na Mbeya.

Miongoni mwa shughuli zilizotekelezwa ni pamoja na Utumishi Marathon 2025 iliyofanyika mkoani Mtwara, Mdahalo wa Kitaifa kuhusu matumizi ya Akili Unde (AI) katika Sekta ya Umma, pamoja na uwekaji wa jiwe la msingi wa mradi wa ujenzi wa Kampasi ya Tanga uliofanywa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mheshimiwa Ridhiwani Jakaya Kikwete (Mb.), tarehe 20 Februari 2026.

Aidha, Chuo kupitia kampasi zake kimefanya shughuli mbalimbali za uwajibikaji kwa jamii, ikiwemo kutoa misaada katika vituo vya kulelea wazee, watoto yatima, watoto wenye mahitaji maalum, vituo vya afya na magereza, pamoja na kutoa elimu ya maadili na uzalendo kwa wanafunzi wa shule za sekondari.

Pia, kwa kushirikiana na Chuo cha Utawala wa Umma Zanzibar, Chuo kiliandaa Kongamano la Pili la Kitaaluma la Utumishi wa Umma Tanzania lililojadili nafasi ya utumishi wa umma katika kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.


Akizungumzia maadhimisho hayo, Dkt. Mabonesho amesema:
"Maadhimisho ya miaka 25 ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania ni fursa muhimu ya kutathmini safari yetu, kuonesha mafanikio tuliyoyapata, kutambua mchango wa wadau wetu, na kuweka mwelekeo wa Chuo katika kuendelea kuimarisha utumishi wa umma wenye weledi, maadili na ufanisi nchini."

Dkt. Mabonesho ameongeza kuwa katika kipindi cha miaka 25, Chuo kimepata mafanikio makubwa ikiwemo kupanua huduma zake kutoka kampasi mbili hadi kampasi sita, kuongeza programu za mafunzo ya muda mfupi na muda mrefu, kuimarisha matumizi ya teknolojia katika utoaji wa mafunzo, pamoja na kuendeleza miundombinu na rasilimali watu.

Mgeni rasmi katika kilele cha maadhimisho hayo anatarajiwa kuwa Mheshimiwa Ridhiwani Jakaya Kikwete (Mb.), Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kinawakaribisha wadau wote wa Chuo, wahitimu, watumishi wa umma, taasisi mbalimbali, sekta binafsi, washirika wa maendeleo na wananchi kwa ujumla kushiriki katika tukio hili muhimu la kihistoria

Na Mwandishi Wetu

Dar es Salaam. Serikali imeendelea kuimarisha mifumo ya ulinzi wa taarifa binafsi nchini ili kuendana na kasi ya maendeleo ya teknolojia za kidijitali, ikisisitiza kuwa faragha ya wananchi ni msingi wa kujenga uchumi wa kidijitali unaoaminika, salama na jumuishi kuelekea Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050.

Msisitizo huo umetolewa leo jijini Dar es Salaam wakati wa ufunguzi wa Kongamano la Kwanza la Faragha na Ulinzi wa Taarifa Binafsi lenye kaulimbiu isemayo, "Faragha ya Taarifa ni Nguzo; Kupata Mustakabali Jumuishi wa Kidijitali Kuelekea Dira 2050." Kongamano hilo limewakutanisha wadau kutoka serikalini, sekta binafsi, wataalamu wa TEHAMA na sheria kujadili namna ya kuimarisha ulinzi wa taarifa binafsi nchini.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kongamano hilo, Naibu Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dkt. Switbert Mkama, alisema taarifa binafsi ni nyenzo muhimu inayomtambulisha mtu na hivyo zinapaswa kulindwa kwa umakini ili kulinda haki, utu na usalama wa wananchi pamoja na kujenga mazingira rafiki kwa wawekezaji katika uchumi wa kidijitali.

Alisema Serikali ilianzisha Tume ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi (PDPC) mwaka 2022 ili kusimamia utekelezaji wa Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi, kutoa elimu kwa umma na kuhakikisha taasisi zote zinazokusanya au kuchakata taarifa za wananchi zinafuata sheria na viwango vinavyotakiwa.

"Uchumi wa kidijitali hauwezi kujengwa kwa teknolojia pekee. Unahitaji uaminifu na usalama wa taarifa zinazochakatwa katika mifumo mbalimbali ya kidijitali. Kadiri huduma za Serikali na sekta binafsi zinavyozidi kuhamia kidijitali, ndivyo ulazima wa kulinda taarifa za wananchi unavyoongezeka," alisema Dkt. Mkama.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi (PDPC), Dkt. Emmanuel Mkilia, alisema kongamano hilo ni la kwanza kufanyika tangu kupitishwa kwa Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi mwaka 2022 na linatoa fursa ya kutathmini mafanikio yaliyopatikana pamoja na kuweka mikakati ya kuimarisha utekelezaji wa sheria hiyo.

Alisema ongezeko la matumizi ya huduma za kidijitali nchini limeongeza kasi ya ukusanyaji na uchakataji wa taarifa binafsi, hali inayohitaji mifumo madhubuti ya kulinda faragha ya wananchi na kujenga imani katika matumizi ya teknolojia.

Dkt. Mkilia alisisitiza kuwa faragha ya taarifa binafsi si kikwazo kwa maendeleo ya uchumi wa kidijitali, bali ni msingi wa kujenga uaminifu, usalama na ukuaji endelevu wa huduma za kidijitali nchini.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Tume ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi, Dkt. Adadi Mohammed Rajabu, alisema maendeleo ya teknolojia, hususan matumizi ya akili mnemba (AI) na huduma za mtandaoni, yamefungua fursa kubwa za ubunifu na uwekezaji, lakini pia yameongeza umuhimu wa kuimarisha ulinzi wa taarifa binafsi bila kuathiri maendeleo ya teknolojia.

Alisema Tanzania inalenga kuwa kitovu cha ulinzi wa taarifa binafsi katika ukanda wa Afrika Mashariki na kimataifa kwa kuhakikisha maendeleo ya kidijitali yanaenda sambamba na heshima ya utu wa binadamu, uwajibikaji na usalama wa taarifa.

Kongamano hilo la siku tatu litakalomalizika Julai 1, 2026 linatarajiwa kuibua mapendekezo, suluhisho na mikakati mipya ya kuimarisha ulinzi wa taarifa binafsi nchini, huku likitoa fursa kwa wadau wa sekta ya TEHAMA, sheria na sekta binafsi kubadilishana uzoefu kuhusu mustakabali wa uchumi wa kidijitali Tanzania.

Naibu Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dkt. Switbert Mkama, akizungumza wakati wa ufunguzi wa Kongamano la Kwanza la Faragha na Ulinzi wa Taarifa Binafsi, lenye kaulimbiu isemayo, "Faragha ya Taarifa ni Nguzo; Kupata Mustakabali Jumuishi wa Kidijitali Kuelekea Dira 2050," lililofanyika leo jijini Dar es Salaam.Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi (PDPC), Dkt. Emmanuel Mkilia, akizungumza wakati wa ufunguzi wa Kongamano la Kwanza la Faragha na Ulinzi wa Taarifa Binafsi, lenye kaulimbiu isemayo, "Faragha ya Taarifa ni Nguzo; Kupata Mustakabali Jumuishi wa Kidijitali Kuelekea Dira 2050," lililofanyika leo jijini Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa Bodi ya Tume hiyo, Dkt. Adadi Mohammed Rajabu akizungumza wakati wa ufunguzi wa Kongamano la Kwanza la Faragha na Ulinzi wa Taarifa Binafsi, lenye kaulimbiu isemayo, "Faragha ya Taarifa ni Nguzo; Kupata Mustakabali Jumuishi wa Kidijitali Kuelekea Dira 2050," lililofanyika leo jijini Dar es Salaam.













Top News