Na Janeth Raphael MichuziTv Bungeni - Dodoma

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Leonard Akwilapo amesema Wizara hiyo imejipanga kuanzisha mabaraza mapya 18 ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya katika mwaka wa fedha 2026/27 ikiwa ni sehemu ya mkakati wa Serikali kuhakikisha huduma za utatuzi wa migogoro ya ardhi zinapatikana katika wilaya zote 139 nchini.

Waziri Dkt. Akwilapo ameyasema hayo bungeni leo  wakati akiwasilisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa mwaka wa fedha 2026/27, akieleza kuwa hatua hiyo inalenga kuongeza upatikanaji wa haki kwa wananchi pamoja na kuharakisha usikilizwaji wa mashauri ya ardhi katika maeneo mbalimbali nchini.

Amesema pamoja na kuanzishwa kwa mabaraza hayo mapya, Wizara itaendelea kushughulikia mashauri 10,782 ya ardhi yaliyobaki kutoka kipindi kilichopita sambamba na mashauri mapya yatakayofunguliwa katika mwaka ujao wa fedha.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, Serikali inaendelea kuweka mkazo katika kuboresha mifumo ya utoaji haki katika sekta ya ardhi kutokana na kuongezeka kwa mahitaji ya wananchi ya kupata suluhisho la migogoro ya ardhi kwa wakati na kwa haki.

“Lengo letu ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya haki karibu yao na kwa wakati. Kuanzishwa kwa mabaraza haya mapya kutasaidia kupunguza mlundikano wa mashauri na kuongeza ufanisi katika usimamizi wa migogoro ya ardhi,” alisema Dkt. Akwilapo.

Katika hotuba yake, Waziri huyo pia aliwataka wenyeviti wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya kuendelea kuzingatia misingi ya weledi, uadilifu na haki wanaposhughulikia mashauri yanayowasilishwa mbele yao ili kuongeza imani ya wananchi kwa taasisi hizo.

Amesisitiza kuwa mwenendo wa utoaji haki katika mashauri ya ardhi unapaswa kuzingatia sheria, uwazi na usawa bila upendeleo, akieleza kuwa wananchi wengi hutegemea mabaraza hayo kama sehemu muhimu ya kupata haki zao katika migogoro ya ardhi na makazi.

Aidha, Dkt. Akwilapo amesema Wizara imeendelea kuimarisha matumizi ya mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika shughuli zake mbalimbali kwa lengo la kuongeza ufanisi wa utendaji kazi na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Alieleza kuwa matumizi ya mifumo hiyo yamechangia kuongeza uwazi na uwajibikaji katika utoaji wa huduma za ardhi pamoja na kuimarisha ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali kupitia mifumo ya kidijitali.

Waziri huyo alibainisha kuwa Serikali itaendelea kuwekeza katika maboresho ya mifumo ya TEHAMA ili kuhakikisha huduma za sekta ya ardhi zinapatikana kwa haraka, kwa urahisi na kwa kuzingatia mahitaji ya wananchi katika maeneo yote nchini.

Hatua hiyo inaelezwa kuwa ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuimarisha sekta ya ardhi nchini, kupunguza migogoro ya ardhi na kuongeza ufanisi katika usimamizi wa rasilimali hiyo muhimu kwa maendeleo ya wananchi na Taifa kwa ujumla.





Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Mahakama ya Rufaa Mhe.Jacobs Mwambegele akizungumza wakati alipotembelea mafunzo ya siku moja kwa Makarani waogozaji Wapiga Kura katika Jimbo la Isimani yaliyofanyika katika Shule Sekondari Ufundi Ifunda mkoani Iringa ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya Uchaguzi huo utakaofanyika Jumatatu ya Juni 1, 2026.





Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Mahakama ya Rufaa Mhe.Jacobs Mwambegele akizungumza wakati alipotembelea mafunzo ya siku moja kwa Makarani waogozaji Wapiga Kura katika Jimbo la Isimani yaliyofanyika katika Shule Sekondari Ufundi Ifunda mkoani Iringa ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya Uchaguzi huo utakaofanyika Jumatatu ya Juni 1, 2026.


Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Mahakama ya Rufaa Mhe.Jacobs Mwambegele amewataka watendaji wa uchaguzi ambao ni Makarani waongozaji Wapiga kura kufanya kazi yao kwa kufuata Sheria, Kanuni na utaratibu wakati wa uchaguzi Mdogo wa Ubunge katika Jimbo la Isimani Mkoani Iringa na Kata 12 za Tanzania Bara.

Jaji Mwambegele ameyasema hayo wakati akitembelea mafunzo ya siku moja kwa Makarani hao waogozaji katika Jimbo la Isimani yaliyofanyika katika Shule Sekondari Ufundi Ifunda mkoani Iringa ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya Uchaguzi huo utakaofanyika Jumatatu ya Juni 1, 2026.

Jaji Mwambegele pia amewasisistiza watendaji hao kuishi kwenye viapo vyao wakati wa utekelezaji majukumu yao ya Uchaguzi ili kujiepusha na upendeleo wa aina yoyote.

Kwa upande wake mwenyekiti wa Mafunzo hayo ya Makarani Waongozaji Wapiga Kura Vituoni Bw. Baraka Matonya amemuhakikishia Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi kwamba watafuata sheria, kanuni, miongozo na maelekezo ya Tume wakati wote wa Utekelezaji wa majukumu yao ya Uchaguzi .

Naye Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Isimani,Bi. Caroline Otieno amesema maandalizi ya uchaguzi huo Mdogo wa Jimbo hilo, yamekamilika kwa asilimia 100 ambapo vifaa vyote vimepokelewa.

Uchaguzi huo utafanyika sambamba na uchaguzi mdogo katika kata 12 za Tanzania Bara ambazo ni Mzimuni iliyopo Manispaa ya Kinondoni; Zongomera, Manispaa ya Kahama; Itilo, Halmashauri ya Mji wa Nzega; Ketare, Halmashauri ya Mji wa Tarime na Nyumbigwa, Halmashauri ya Mji wa Kasulu.

Nyingine ni kata ya Kala iliyoko Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi; Ziba, Halmashauri ya Wilaya Igunga; Kamsisi, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele; Nyamugali, Halmashauri ya wilaya ya Buhigwe; Namasakata Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru; Bwongera, Halmashauri ya Wilaya ya Chato na Kibiti Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti.





Sehemu ya washiriki wa mafunzo hayo wakimsikiliza Mwenyekiti wa Tume.

Mratibu wa Uchaguzi Mkoa wa Iringa Bi. Nuru Sovella akizungumza wakati wa mafunzo hayo.
Sehemu ya washiriki wa mafunzo hayo wakimsikiliza Mwenyekiti wa Tume.

Sehemu ya washiriki wa mafunzo hayo wakimsikiliza Mwenyekiti wa Tume.

Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Isimani,Bi. Caroline Otieno akizungumza na kusema kua maandalizi ya uchaguzi huo Mdogo wa Jimbo hilo, yamekamilika kwa asilimia 100 ambapo vifaa vyote vimepokelewa.

Na Byera Deus-Bukoba.

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa TAKUKURU Mkoa wa Kagera, imewaomba madiwani kujiunga na mpango wa TAKUKURU Rafiki unaolenga kuzuia rushwa katika jamii kwa njia ya mazungumzo na utatuzi wa kero.

Katika semina fupi iliyoandaliwa na TAKUKURU Mkoa wa Kagera, iliyowakutanisha madiwani, watendaji pamoja na watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Bukoba kwa lengo la kujadili uwajibikaji na wajibu wa viongozi katika suala la kuzuia rushwa, Naibu Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Kagera, Leonard Swai, alisema kuwa mpango wa TAKUKURU Rafiki unalenga kuokoa miradi na kumaliza rushwa kwa njia ya mazungumzo.

Alisema changamoto kubwa iliyopo kwa sasa ni malalamiko juu ya miradi, ambapo malalamiko hayo hutolewa baada ya mradi kufika hatua za mwisho, wakati kinachotakiwa ni kumaliza tatizo kabla ya mradi kutekelezwa hadi mwisho. Amewataka madiwani kushiriki katika mpango huo ili kuokoa miradi ya maendeleo inayogusa wananchi wao.

“Tusisubiri mpaka watu wakamatwe kwenda mahakamani, huko kuna sheria ngumu, ni vizuri tukawa timu tukashauriana, na mara nyingi wananchi mpaka kufika kwetu wanakuwa wamepitia kero ambazo hazina majibu. Ni vizuri madiwani, wakuu wa idara pamoja na watendaji wakishirikiana vizuri sana wataepusha changamoto nyingi na hakuna mradi ambao utapotea.”

Aidha, alisema wajibu mwingine wa madiwani, pamoja na kusimamia jamii, ni kuendelea kuwasimamia watendaji pamoja na watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Bukoba katika suala zima la ukusanyaji wa mapato ili kuongeza ufanisi wa mapato ya ndani na kuiwezesha halmashauri kujiendesha kwa ufanisi zaidi, pia aliwataka watendaji kuacha tabia za kukaanga fedha wanazokusanya kwenye vyanzo vya mapato ili wasipelekwe mahakamani.

Kwa upande wao, baadhi ya madiwani walieleza kuwa semina hiyo imewapa uelewa mpana kuhusu masuala ya rushwa na kudai kuwa wanapaswa kushirikishwa katika miradi ya maendeleo ili waweze kuibua vitendo vya rushwa mapema kwa njia rafiki na kuwezesha miradi kukamilika kwa wakati.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Bukoba, Fatina Hussein Laay, alisema kuwa mpango wa TAKUKURU Rafiki ni mpango mzuri kwani unalenga kufanya uchambuzi wa makosa gani yanapaswa kupelekwa mahakamani au kujadiliwa kwa njia rafiki, ameishukuru TAKUKURU kwa mafunzo kwa madiwani kwani wao ndio wasimamizi wakubwa wa maendeleo ya kata.









Na Karama Kenyunko Michuzi Tv


MAHAKAMA Kuu Masjala Ndogo Dar es Salaam imeitupilia mbali kesi ya mgogoro wa mgawanyo wa rasilimali kati ya Tanzania Bara na Zanzibar iliyokuwa ikiikabili Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), baada ya kuridhika kuwa hati ya madai ilikuwa na kasoro za kisheria.

Uamuzi huo umetolewa leo Mei 28, 2026 na Jaji David Ngunyale aliyekubaliana na pingamizi la awali lililowasilishwa na Chadema kuwa wadai walishindwa kubainisha muda rasmi ambao madai yao yalitokea kama inavyotakiwa kisheria.

Katika uamuzi wake, Jaji Ngunyale alisema baada ya kupitia hati ya madai alibaini kuwa baadhi ya matukio yalitajwa kwa ujumla kwa miaka ya 2014 na 2019 bila kuonesha tarehe rasmi ambazo mgogoro huo ulianza.

Alisema Amri ya VII kanuni ya 1(e) ya Kanuni za Mwenendo wa Mashauri ya Madai (CPC) inataka mlalamikaji kubainisha muda ambao sababu ya madai ilitokea ili mahakama iweze kujiridhisha kama kesi imefunguliwa ndani ya muda unaotakiwa kisheria.

“Hivyo mahakama inashindwa kujiridhisha kama ina mamlaka ya kuisikiliza kesi hii au la. Kitendo cha mahakama kushindwa kuona mgogoro ulianza lini ni upungufu ambao mahakama inayosimamia sheria haiwezi kuuacha hivihivi,” alisema Jaji Ngunyale.

Kutokana na sababu hizo, mahakama ilitupilia mbali kesi hiyo huku ikielekeza kila upande kubeba gharama zake.

Kesi hiyo ya madai namba 8323 ya mwaka 2025 ilikuwa imefunguliwa na Makamu Mwenyekiti mstaafu wa Chadema, Said Issa Mohamed pamoja na wajumbe wawili wa Bodi ya Wadhamini wa chama hicho kutoka Zanzibar, Ahmed Rashid Khamis na Maulida Anna Komu.

Waliofunguliwa kesi walikuwa ni Bodi ya Wadhamini Waliosajiliwa wa Chadema na Katibu Mkuu wa chama hicho.

Katika madai yao, wadai walidai kuwa kumekuwa na mgawanyo usio sawa wa mali na rasilimali za kifedha za chama kati ya Tanzania Bara na Zanzibar kinyume na Sheria ya Vyama vya Siasa pamoja na Katiba ya Chadema.

Pia walidai kuwepo kwa ubaguzi wa kidini na kijinsia pamoja na matamko yenye nia ya kuvuruga Muungano wa Tanzania.

Mbali na madai hayo, waliomba mahakama kusitisha shughuli zote za kisiasa za chama hicho pamoja na matumizi ya mali na fedha zake hadi maagizo ya mahakama yatakapotekelezwa.

Awali, upande wa wadaiwa uliwasilisha pingamizi la awali ukidai kesi hiyo ilikuwa na kasoro za kisheria pamoja na kufunguliwa nje ya muda uliowekwa na sheria.

Kiongozi wa jopo la mawakili wa wadaiwa, Mpale Mpoki, alidai kuwa hati ya madai haikuonesha ni lini sababu ya madai ilitokea jambo lililoifanya mahakama ishindwe kutambua kama kesi imefunguliwa ndani ya muda au la.

Alisema matakwa ya Amri ya VII kanuni ya 1(e) ya CPC yanahitaji mlalamikaji kueleza wazi muda wa kutokea kwa madai hayo.

Upande wa wadai ukiongozwa na wakili Shabani Marijani ulidai kuwa hati ya madai ilikuwa imeeleza matukio mbalimbali katika aya ya saba hadi ya 16 na kwamba baadhi yake yalikuwa yanaendelea hadi sasa.

Hata hivyo, mawakili wa Chadema walisisitiza kuwa maelezo hayo hayakubainisha tarehe rasmi ya kuanza kwa mgogoro huo.

Kabla ya uamuzi huo, Mahakama ya Rufani Aprili 15, 2026 ilibatilisha sehemu ya uamuzi wa Mahakama Kuu uliokuwa umekizuia chama hicho kufanya shughuli za kisiasa na kutumia mali zake hadi kesi ya msingi itakaposikilizwa.

Mahakama ya Rufani pia ilielekeza kesi hiyo isikilizwe na jaji mwingine tofauti na Jaji Hamidu Mwanga aliyekuwa akiisikiliza awali na kuagiza pingamizi kuhusu ukomo wa muda lisikilizwe kwanza.

Kutokana na uamuzi wa leo, shauri la maombi lililokuwa limewasilishwa na Mwenyekiti wa Chadema, Tundu Lissu, nalo limekoma kwa kuwa lilitegemea uwepo wa kesi hiyo ya msingi.



 


Na Oscar Assenga, Tanga

MAMLAKA ya Bandari Tanzania (TPA) imesema kuanzishwa kwa tozo mpya ya maendeleo ya miundombinu ya bandari kutasaidia kuongeza uwezo wa bandari nchini kuhudumia shehena, kupunguza gharama kwa wafanyabiashara na kuchochea ukuaji wa uchumi.

Akizungumza jijini Tanga juzi katika mkutano wa wadau wa watumiaji wa Bandari ya Tanga kuhusu ada ya maendeleo ya miundombinu ya bandari, Meneja wa Bandari ya Tanga, Salehe Mbega, alisema tozo hiyo inayojulikana kama Port Infrastructure Development Levy (PID) ilitarajiwa kuanza kutumika Machi mwaka huu, lakini imeahirishwa hadi Julai Mosi kufuatia maoni ya wadau mbalimbali.

Mkutano huo ulihudhuriwa na wadau mbalimbali, wakiwemo wanachama wa Chama cha Mawakala wa Forodha Tanzania (TACAS), ambao waliunga mkono tozo hiyo wakisema italeta mageuzi makubwa katika utoaji wa huduma bandarini nchini.

Mbega alisema lengo la tozo hiyo ni kuboresha miundombinu ya bandari ambayo imeanza kuelemewa kutokana na ongezeko kubwa la shehena katika bandari za Tanga, Dar es Salaam na Mtwara.

“Bandari ya Tanga kwa sasa inahudumia takribani tani milioni mbili za shehena kwa mwaka, wakati uwezo wa miundombinu iliyopo unatarajiwa kufikia tani milioni tatu ifikapo mwaka 2030. Hata hivyo, kutokana na kasi ya ukuaji wa shehena, kiwango hicho kinaweza kufikiwa mapema mwaka 2027 au 2028,” alisema Mbega.

Alisema Serikali kwa kushirikiana na wadau wa sekta ya usafirishaji imeona umuhimu wa kuwekeza zaidi katika miundombinu ili bandari ziweze kuhimili ongezeko la mizigo.

Mbega alisema fedha zitakazokusanywa kupitia tozo hiyo zitatumika kujenga na kuboresha miundombinu mbalimbali, ikiwemo kuongeza gati jipya katika Bandari ya Tanga.

“Kwa sasa tuna magati mawili, lakini tuna mpango wa kuongeza gati la tatu lenye urefu wa mita 900. Pia eneo la Mwambani lina nafasi kubwa ya kujengwa bandari mpya yenye zaidi ya magati 10 katika eneo la ekari 174,” alisema.

Aliongeza kuwa maboresho hayo yataongeza uwezo wa nchi kuhudumia shehena nyingi zaidi na kuifanya Tanzania kuwa kitovu muhimu cha biashara katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Kwa mujibu wa Mbega, tozo hiyo pia itasaidia kupunguza gharama wanazopata wafanyabiashara kutokana na ucheleweshaji wa huduma bandarini.

Alisema baadhi ya meli hulazimika kusubiri nje ya bandari kwa muda wa wiki tatu hadi mwezi mmoja kabla ya kuhudumiwa, hali inayosababisha hasara kubwa kwa wafanyabiashara.

“Meli inapokaa nje ya bandari hulipiwa hadi dola za Marekani 20,000 kwa siku. Ukihesabu kwa mwezi mzima ni gharama kubwa sana kwa wafanyabiashara. Tozo hii itasaidia kuongeza ufanisi na kupunguza mzigo huo,” alisema.

Aidha, Mbega alisema maboresho yaliyofanywa kwenye reli ya Tanga kwa gharama ya Sh bilioni 429.1 yameongeza usafirishaji wa mizigo kwenda Rwanda na Burundi.

Alisema reli hiyo ambayo kwa muda mrefu ilikuwa haitumiki sasa imefunguliwa na kuanza kupokea shehena nyingi kutoka bandarini kwenda Isaka kabla ya kusafirishwa kwenda nchi hizo jirani.

Hata hivyo, alisema ongezeko la mahitaji ya usafirishaji kwa njia ya reli limezidi uwezo wa mabehewa yaliyopo.


“Wateja wanaopendelea kutumia reli wameongezeka zaidi kuliko uwezo wa mabehewa yaliyopo. Huu ni wakati sahihi kwa sekta ya reli kuongeza mabehewa ili kukidhi mahitaji ya soko,” alisema.

Awali akizungumza katika mkutano huo, Mwenyekiti wa TACAS, Ephraim Mwankusye, alisema pendekezo la ada ya asilimia 4.5 ya maendeleo ya miundombinu ya bandari lina lengo la kusaidia maboresho makubwa ya bandari nchini ili kuongeza ufanisi wa huduma za usafirishaji wa mizigo.

Alisema fedha zitakazopatikana zitaelekezwa katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kuendeleza Bandari za Dar es Salaam, Tanga, Mtwara pamoja na Bandari ya Bagamoyo na ujenzi wa miundombinu ya mafuta katika bandari mbalimbali nchini.

Mwankusye alisema lengo kubwa ni kuhakikisha bandari za Tanzania zinakuwa za kisasa, zenye uwezo mkubwa wa kuhudumia mizigo mingi kwa haraka na kwa ufanisi zaidi.

Kwa mujibu wa pendekezo hilo, asilimia 4.5 ya tozo ya PID itaelekezwa katika miradi ya kuboresha bandari, magati, reli, matenki ya mafuta pamoja na barabara zinazosaidia usafirishaji wa mizigo.



Na Janeth Raphael MichuziTv Bungeni - Dodoma

Mbunge wa Korogwe Vijijini, Timotheo Mnzava, ameishauri Serikali kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuharakisha uimarishaji na usambazaji wa mfumo wa kidijitali wa usimamizi wa ardhi nchini ili kupunguza migogoro ya ardhi na kuongeza ufanisi katika ukusanyaji wa mapato ya Serikali.

Akizungumza bungeni leo wakati akichangia mjadala wa Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa mwaka wa fedha 2026/27, Mnzava amesema kuwa licha ya Serikali kuanza hatua za matumizi ya mifumo ya kidijitali katika usimamizi wa ardhi, bado halmashauri chache pekee ndizo zimefanikiwa kufikiwa na mfumo huo, jambo linalochangia kuendelea kuwepo kwa migogoro ya ardhi katika maeneo mbalimbali nchini.

Amesema mfumo huo unapaswa kusambazwa katika halmashauri zote nchini ili kurahisisha usimamizi wa taarifa za ardhi, kuongeza uwazi katika umiliki wa maeneo na kusaidia wananchi kupata huduma kwa haraka zaidi.

“Mpaka sasa ni halmashauri chache sana ambazo zimefanikiwa kupata mfumo wa kidijitali wa usimamizi wa ardhi. Serikali inapaswa kuhakikisha mfumo huu unasambazwa nchi nzima ili kupunguza migogoro ya ardhi na kuongeza ufanisi katika sekta hii muhimu,” amwsema Mzava.

Mbunge huyo alikiri kuwa utekelezaji wa mpango huo unahitaji fedha nyingi, lakini akasisitiza kuwa umuhimu wa sekta ya ardhi kwa uchumi wa taifa unapaswa kupewa kipaumbele maalum.

Amesema mapato yanayotokana na kodi na pango la ardhi yanaweza kutumika kusaidia kuendeleza mifumo hiyo ya kisasa, huku akiishauri Serikali kuhakikisha sehemu ya fedha zinazokusanywa na Wizara ya Ardhi zinabaki wizara hiyo ili kusaidia kuimarisha mifumo ya usimamizi na kuongeza uwezo wa ukusanyaji wa mapato zaidi.

“Kazi ya kusambaza mfumo huu nchi nzima siyo ndogo, ninafahamu kutakuwa na changamoto ya upatikanaji wa fedha. Lakini kutokana na umuhimu wa sekta ya ardhi, naiomba Serikali mapato yanayotokana na kodi na pango la ardhi yarudishwe kwa kiwango kikubwa zaidi wizara husika ili waweze kuendelea kutengeneza mifumo na kuboresha ukusanyaji wa mapato,” amesisitiza.

Mnzava ameeleza kuwa katika baadhi ya nchi zilizoendelea, sekta ya ardhi imekuwa chanzo kikubwa cha mapato ya Serikali kupitia kodi mbalimbali zinazotokana na umiliki na matumizi ya ardhi, hivyo Tanzania nayo inaweza kunufaika zaidi iwapo itawekeza vya kutosha katika mifumo ya kisasa ya usimamizi wa ardhi.

Aidha, ameipongeza Wizara ya Ardhi kwa juhudi zake za kuongeza makusanyo ya mapato na kuendelea kuboresha huduma kwa wananchi, huku akiitaka Serikali kuendelea kuiwezesha wizara hiyo ili iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi zaidi.

“Tunaona kazi kubwa inayofanywa na Wizara ya Ardhi katika kuongeza makusanyo ya Serikali. Sasa ni wakati wa Serikali kuendelea kupeleka fedha zaidi kwa wizara hiyo ili waweze kufanya kazi kwa ufanisi na kuendelea kulitumikia taifa,” alisema.

Kauli ya mbunge huyo imekuja wakati ambapo Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha matumizi ya teknolojia katika utoaji wa huduma za umma, ikiwa ni pamoja na usimamizi wa ardhi na upangaji wa matumizi bora ya maeneo nchini.


Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) limetangaza rasmi nafasi za mafunzo ya mujibu wa sheria kwa vijana waliohitimu kidato cha sita mwaka 2026, huku likiwataka wote waliopangiwa kuripoti kambini kati ya Juni 1 hadi 7 mwaka huu.

Taarifa hiyo imetolewa na Mkuu wa Tawi la Utawala wa JKT, Brigedia Jenerali Hassan Mabena, kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa, ambapo amesema maandalizi yote ya kuwapokea vijana hao katika kambi mbalimbali nchini yamekamilika.

Amesema mafunzo hayo yanalenga kuwajengea vijana uzalendo, nidhamu, uwezo wa kujitegemea pamoja na kuwapa stadi mbalimbali zitakazowasaidia katika maisha na maendeleo ya taifa.

“Lengo letu ni kuhakikisha vijana wanapata mafunzo yatakayowajenga kuwa wazalendo, wenye maadili mema na uwezo wa kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo ya nchi,” alisema Brigedia Jenerali Mabena.

Ameeleza kuwa JKT itaendelea kuwa sehemu muhimu ya kuwalea vijana katika misingi ya uwajibikaji, mshikamano wa kitaifa na kuthamini amani ya Tanzania.

Kwa mujibu wa Brigedia Jenerali Mabena, wahitimu wote wanatakiwa kuangalia majina yao pamoja na kambi walizopangiwa kupitia tovuti rasmi ya JKT ambayo ni JKT Tanzania.

Aidha, amesema Serikali kupitia bajeti ya mwaka huu imeiwezesha JKT kupokea idadi kubwa ya vijana kutoka Tanzania Bara na Zanzibar kwa ajili ya mafunzo hayo.

Pia amewataka wazazi na walezi kuwapa ushirikiano vijana hao kwa kuwahamasisha kwenda kuripoti kambini ndani ya muda uliopangwa.

“Tunawaomba wazazi na walezi kuhakikisha vijana wanaripoti kwa wakati ili waweze kupata mafunzo haya muhimu kwa mustakabali wao na taifa kwa ujumla,” alisema.

Katika hatua nyingine, Brigedia Jenerali Mabena amesema vijana wenye mahitaji maalum wanapaswa kuripoti katika Kambi ya Ruvu JKT wakiwa na vifaa na nyaraka muhimu zilizoelekezwa na jeshi hilo.

Amesisitiza kuwa vijana wote waliopangiwa wanapaswa kufuata maelekezo yaliyotolewa na kuripoti katika kambi zao ndani ya muda uliopangwa ili kuepusha usumbufu wa kiutawala.



Na Karama Kenyunko, Michuzi TV

SHIRIKA lisilo la Kiserikali la masuala ya Afya ya Uzazi, MSI Tanzania, limeingiza rasmi Tuzo ya Uandishi wa Habari za Afya ya Uzazi katika Tuzo za Umahiri wa Uandishi wa Habari Tanzania (EJAT) 2025, hatua inayolenga kuhamasisha uandishi wa habari za afya wenye manufaa kwa jamii.

Tuzo hiyo ni miongoni mwa makundi mapya yaliyoanzishwa mwaka huu na Baraza la Habari Tanzania (MCT), ikiwa ni sehemu ya maboresho yanayolenga kuendana na mabadiliko ya mazingira ya habari na kuhimiza uandishi wenye utaalamu maalumu.

Hatua hiyo imetangazwa leo Mei 28, 2026 wakati MCT ikiongeza wateule 12 wa EJAT 2025, hatua iliyopanua orodha ya waandishi wa habari na taasisi zinazotambuliwa kwa umahiri wa kitaaluma, maadili ya uandishi na mchango kwa jamii.

Miongoni mwa wateule hao ni Julius Maricha wa The Citizen, Halima Mlacha wa Habari Leo, Hamadi Rashid wa The Loyal Media na UN Radio, Leonard Mubale wa TriGen Media, Philip Mwihava wa Clouds FM na Manyerere Jackton wa Jamhuri Media.

Kwa upande wa taasisi za habari, Azam Media, Nukta Africa, Mwananchi Newspaper, The Guardian Newspaper, Tanzania Standard Newspapers (TSN) na Jamhuri Newspaper zimetajwa kuingia hatua ya mwisho ya tuzo hizo.

Katibu Mtendaji wa MCT, Ernest Sungura, amesema mfumo ulioboreshwa wa tuzo hizo unalenga kuongeza uwakilishi mpana zaidi, hususan katika uandishi wa habari za kidijitali, taarifa za mikoani na miradi ya uchunguzi wa habari.

Mbali na Tuzo ya Afya ya Uzazi, makundi mengine mapya ni Tuzo ya Uandishi wa Habari za Elimu ya Uwezo Tanzania, Tuzo ya Mahojiano Bora ya Mwaka, Tuzo ya Taasisi ya Habari Inayozingatia Sheria kwa Ubora wa Mwaka, Tuzo ya Taasisi ya Habari Yenye Utaalamu Maalumu wa Mwaka, Tuzo ya Uhifadhi ya Mwalimu Julius Nyerere pamoja na Tuzo ya Kijana Chipukizi.

Mkurugenzi Mkazi wa MSI Tanzania, Patrick Kinemo, amesema taasisi hiyo imekuwa ikisaidia programu za afya ya uzazi tangu mwaka 1989 kwa kushirikiana na Wizara ya Afya katika kuboresha huduma za uzazi wa mpango, hasa maeneo yenye changamoto ya upatikanaji wa huduma.

Amesema MSI inaamini mchango wa vyombo vya habari ni muhimu katika kuhakikisha jamii inapata taarifa sahihi kuhusu afya ya uzazi.

Kwa mujibu wa Kinemo, katika kipindi cha miaka minne iliyopita ushirikiano kati ya MSI na MCT umewezesha mafunzo kwa wanahabari 30 na kuchangia kuandaliwa kwa zaidi ya habari 100 kuhusu afya ya uzazi zilizofikia wananchi na watunga sera.
Alisema ushirikiano huo umeongeza uelewa wa jamii kuhusu huduma za afya ya uzazi na kusaidia wananchi wengi, hususan wa maeneo ya mbali, kupata huduma muhimu.

Washindi wa EJAT 2025 wanatarajiwa kutangazwa kesho Mei 29 katika hafla itakayofanyika Hoteli ya Four Points by Sheraton jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mkazi wa MSI Tanzania, Patrick Kinemo akizungumza wakati wa kutangaza kuingizwa kwa Tuzo ya afya ya Uzazi katika tuzo za EJAT 2025 Zimazotarajiwa kutolewa kesho Mei 29, 2026 jijini Dar es Salaam.





Na Mwandishi Wetu, Pwani

WAKALA wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) umesema maboresho ya miundombinu yanayotekelezwa kupitia Mradi wa Kujenga Ustahimilivu wa Bioanuwai ya Misitu dhidi ya Athari za Mabadiliko ya Tabianchi katika Misitu ya Asilia ya Hifadhi Tanzania (BUREFOBI-NFR), yamechochea ukuaji wa utalii ikolojia katika Hifadhi ya Msitu wa Asili wa Pugu Kazimzumbwi, mkoani Pwani.

Hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za Serikali kufikia lengo la kuongeza idadi ya watalii hadi milioni nane ifikapo mwaka 2030 kupitia uboreshaji wa vivutio na huduma za utalii nchini.

Akizungumza wakati wa ziara ya Mshauri wa Kanda wa Shirika la Mpango wa Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), Onesimus Muhwezi, Mratibu wa Mradi wa BUREFOBI-NFR ambaye pia ni Mhifadhi Mkuu wa TFS, Someni Mteleka, alisema uwekezaji huo umeongeza mvuto wa hifadhi hiyo kwa watalii wa ndani na nje ya nchi.

Alisema kupitia ufadhili wa pamoja wa Mfuko wa Mazingira Duniani (GEF) na UNDP, TFS imetekeleza miradi mbalimbali ya kuboresha miundombinu ya utalii katika hifadhi hiyo, ikiwemo ujenzi wa barabara ya kilomita 12 katika eneo la Kimani–Maguruwe, mabanda mawili ya kupumzikia watalii pamoja na lango la kuingilia hifadhini.

“Uboreshaji huu umeongeza upatikanaji wa huduma na kurahisisha watalii kufikia maeneo mbalimbali ya vivutio ndani ya hifadhi,” alisema Mteleka.

Alibainisha kuwa kati ya mwaka 2020 na 2025, Hifadhi ya Pugu Kazimzumbwi imerekodi ongezeko la wastani wa watalii kwa asilimia 69, hali aliyosema imechangiwa na uwekezaji katika miundombinu ya utalii ikolojia na ushirikiano kati ya Serikali na washirika wa maendeleo.

Kwa upande wake, Muhwezi aliipongeza Serikali ya Tanzania kwa usimamizi mzuri wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa kupitia ufadhili wa washirika wa kimataifa, akisema miradi hiyo imekuwa na mchango mkubwa katika uhifadhi wa mifumo ya ikolojia, kukuza uchumi wa jamii zinazozunguka hifadhi pamoja na kuongeza mapato yatokanayo na utalii.

Hifadhi ya Msitu wa Asili wa Pugu Kazimzumbwi ni miongoni mwa hifadhi tisa zinazotekelezwa mradi wa BUREFOBI-NFR, unaolenga kuimarisha ustahimilivu wa bioanuwai ya misitu dhidi ya athari za mabadiliko ya tabianchi nchini.




Balozi wa Tanzania nchini Algeria, Mhe. Mobhare Matinyi, akiwasilisha nakala za hati za utambulisho kwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Algeria, Mhe. Ahmed Attaf, jijini Algiers, leo tarehe 26 Mei, 2026.

Balozi wa Tanzania nchini Algeria, Mhe. Mobhare Matinyi, akiwa katika mazungumzo mafupi na Waziri wa Mambo ya Nje wa Algeria, Mhe. Ahmed Attaf, mara baada ya kuwasilisha nakala za hati za utambulisho jijini Algiers, leo tarehe 26 Mei, 2026. Mazungumzo hayo yalihusu uimarishaji wa ushirikiano na uhusiano baina ya nchi hizi mbili.

Na Mwandishi wetu, Simanjiro
HALMSHAURI ya Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara, baada ya kupata mradi wa mpango wa kukabiliana na mabadiliko ya Tabianchi (SCALE), wataalamu mbalimbali wamekuwa wakipita maeneo tofauti yatakayonufaika na mpango huo kwa kutoa elimu kwa jamii.


Wananchi wa Kijiji cha Olchoronyori Kata ya Msitu wa Tembo, wamepatiwa elimu endelevu kuhusu mbinu za kuhimili na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi, ikiwa ni mkakati wa kujenga jamii inayostahimili majanga ya kimazingira.

Elimu hiyo imetolewa kupitia Mpango wa Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi (SCALE), kwa kipindi cha miaka mitano. Lengo likiwa ni kuwajengea wananchi uelewa wa namna ya kuzuia na kukabiliana na majanga kama vile ukame wa muda mrefu, mafuriko, milipuko ya magonjwa, pamoja na tishio la njaa.

Akizungumza katika mkutano wa wananchi uliofanyika katika kijiji hicho mwezeshaji wa mafunzo hayo mhandisi Joanes Martine amewataka wananchi kuwa mabalozi wema katika jamii zao kwa kuhakikisha wanasimamia sheria na taratibu za utunzaji wa mazingira.

“Nawasihi mkawe mabalozi katika jamii zenu. Shirikianeni kwa pamoja kufuata kanuni bora za utunzaji wa mazingira ikiwemo upandaji wa miti, kilimo endelevu, na kukomesha kabisa tabia ya ukataji miti ovyo pamoja na uchomaji mkaa,” alisisitiza mhandisi Joanes.

Pia, mwezeshaji huyo amewataka wananchi kuwa mstari wa mbele katika kuchochea maendeleo kwa kuibua miradi na fursa mpya zitakazovutia uwekezaji zaidi kutoka serikalini, hatua itakayosaidia kukuza uchumi wa jamii hiyo na taifa kwa ujumla.

Hata hivyo, mpango huo unafanyika kwa kuratibiwa na timu ya mabadiliko ya tabianchi kutoka ngazi ya Halmashauri (CCAT) kwa kushirikiana na timu ya mabadiliko ya tabianchi ngazi ya kata (WCAT).

Kata sita za Oljoro namba tano, Shambarai, Msitu wa Tembo, Loiborsoit, Ruvu Remit na Kitwai zinatarajiwa kunufaika na mradi huo wa SCALE.

Mradi huo wa SCALE unatekelezwa katika mikoa 21 ya Tanzania bara katika halmshauri 54 na mikoa mitano ya Zanzibar kwenye Halmashauri 11.


BARAZA la Madiwani la Halmashauri ya Jiji la Dodoma limewafukuza kazi watumishi watatu na mtumishi mmoja kushushwa cheo na mshahara kufuatia kukiuka misingi na taratibu za Utumishi wa Umma.

Maamuzi hayo yalifanyika katika Mkutano maalum wa Mashauri ya Kinidhamu uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Watumishi waliofukuzwa kazi ni Afisa Muuguzi Msaidizi, Muuguzi na Afisa Mtendaji wa Mtaa. Mtumishi aliyeshushwa cheo na mshahara ni Mteknolojia Maabara.

Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Alimwoni Chaula alilihoji Baraza la Madiwani, na kwa kauli moja liliridhia kuwafukuza kazi watumishi hao watatu na kushushwa cheo na mshahara mtumishi mmoja.

Akiwasilisha taarifa ya kuhitimisha mashauri ya nidhamu ya watumishi wanne kwa Baraza maalum la Mashauri ya Nidhamu, Mkuu wa Divisheni ya Utawala na Menejimenti ya Rasilimali watu kwa niaba ya Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma, Gerald Ruzika alisema kuwa mkurugenzi aliunda kamati ya uchunguzi kwa mujibu wa Kanuni ya 45 na 46 ya Kanuni za Utumishi wa Umma za Mwaka 2022 kuchunguza tuhuma dhidi ya watumishi wanne.

Akiongelea mashtaka waliyotuhumiwa nayo alisema kuwa Mteknolojia Maabara alishtakiwa kwa kushindwa kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi kwa sababu ya matumizi ya pombe yaliyokithiri, kutumia bila idhini ya mamlaka vifaa vya umma kwa shughuli zisizohusiana na majukumu yake, kufanya mambo ambayo yanashusha hadhi ya Utumishi wa Umma, kwenda kinyume na maadili ya Utumishi wa Umma na kutokuwepo kazini kwa zaidi ya siku tano bila kuwa na likizo ama ruhusa ya mwajiri.

Kwa upande wa Afisa Muuguzi Msaidizi alishtakiwa kwa kutokuwepo kazini kwa zaidi ya siku tano bila kuwa likizo au ruhusa ya mwajiri.

Muuguzi alishtakiwa kwa kutokuwepo kazini kwa zaidi ya siku tano bila kuwa likizo, ruhusa ya mwajiri au sababu za msingi na kutofanya majukumu aliyopangiwa kama mtumishi wa umma.

Mtendaji wa Mtaa alishtakiwa kwa kutokuwepo kazini bila kuwa likizo, ruhusa au sababu za msingi na kutotekeleza majukumu aliyopangiwa kama mtumishi wa umma.







MKURUGENZI Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, Bi. Erica Yegela, ametembelea banda la Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya (MZRH) katika Maonesho ya Nne ya Biashara na Kilimo (Mbeya City Expo 2026) yanayofanyika kwenye viwanja vya lililokuwa Soko la Zamani la Uhindini Jijini Mbeya.

Akiwa bandani hapo, Bi. Yegela amejionea namna wataalamu wa afya wanavyotoa huduma mbalimbali za kibingwa na kibobezi bila malipo kwa wananchi wanaofika kujitokeza kwenye maonesho hayo makubwa Nyanda za Juu Kusini.

Bi. Yegela ameupongeza Uongozi wa hospitali hiyo chini ya Mkurugenzi Mtendaji, Dkt. Godlove Mbwanji, kwa kusogeza huduma za kisasa na vipimo vya kibingwa karibu na jamii, hatua inayookoa muda na gharama kwa wananchi wa mkoa wa Mbeya na mikoa jirani.

"Nimefarijika sana kuona namna hospitali yetu ya kanda ilivyojipanga vizuri kusogeza huduma hizi kubwa na muhimu hapa kiwanjani. Wananchi wasisubiri hadi wawe wagonjwa sana, waje sasa hivi kupata ushauri na vipimo kutoka kwa madaktari bingwa," alisema Bi. Yegela.

Aidha, ametoa wito kwa wakazi wote wa Mbeya na maeneo ya jirani kujitokeza kwa wingi katika maonesho hayo kuanzia sasa hadi yatakapotamatika tarehe 30 Mei 2026, ili kupata huduma bora za afya pamoja na kujifunza fursa mbalimbali za biashara na kilimo zilizopo mkoani hapo.

Amesema kuwa uwepo wa huduma hizo bure ni fursa ya kipekee ambayo haipaswi kuachwa hivi hivi na wananchi wanaojali afya zao.

Maonesho hayo ya Mbeya City Expo yameandaliwa na Chemba ya Biashara, Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA) kwa ushirikiano na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, yakiwa na lengo la kukuza uchumi, biashara, kilimo, na uwekezaji mkoani humo.

Hadi sasa, maonesho hayo yamevutia taasisi nyingi za kiserikali na binafsi zinazotoa elimu na huduma mbalimbali kwa umma.






📍Mtwara

Mkoa wa Mtwara umeendelea kujidhihirisha kama kitovu muhimu cha uwekezaji wa madini nchini kutokana na uwepo wa rasilimali nyingi za madini ya viwandani, vito na madini mkakati, huku mapato ya Serikali kupitia sekta hiyo yakiongezeka kwa kasi katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita.

Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Mtwara, Winnifrida Mrema, amesema mkoa huo unafahamika zaidi kwa uwepo wa madini ya chokaa yanayotumika kuzalisha saruji katika Kiwanda cha Saruji cha Dangote, jambo linalochangia kukuza uchumi wa mkoa na kuimarisha shughuli za viwanda nchini.

Amesema Mkoa wa Mtwara pia una utajiri wa madini mengine ya viwandani yakiwemo chuma, shaba, kinywe, ulanga pamoja na madini ya mchanga mzito (heavy mineral sands), ambayo ni miongoni mwa madini mkakati yanayohitajika kwa kiwango kikubwa duniani katika utengenezaji wa teknolojia mbalimbali ikiwemo magari ya umeme.

Aidha, amesema Bandari ya Mtwara imeendelea kuwa kiungo muhimu cha biashara na usafirishaji wa madini na bidhaa za viwandani, ambapo hutumika kusafirisha saruji ya Dangote kwenda Zanzibar na Visiwa vya Comoro, sambamba na usafirishaji wa makaa ya mawe kutoka mikoa ya Ruvuma na Njombe kuelekea masoko ya China, India na Dubai.

Kwa upande wa uwekezaji, Mrema amesema Mkoa wa Mtwara una fursa kubwa katika uchimbaji na uchakataji wa madini ya dhahabu, shaba pamoja na vito, hususan green garnet, huku akiwahimiza wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kutumia fursa hizo kuwekeza katika sekta ya madini.

Pia amesema Serikali inaendelea kuwahamasisha wawekezaji kushirikiana na wachimbaji wadogo wa madini ya viwandani, dhahabu na vito kwa kuwapatia mitaji, mafunzo na msaada wa kitaalam ili kuongeza uzalishaji na kuboresha shughuli zao za uchimbaji.

Akizungumzia mapato ya Serikali, Mrema amesema makusanyo kupitia sekta ya madini mkoani humo yameongezeka kutoka shilingi bilioni 1.85 mwaka 2021/22 hadi shilingi bilioni 5.95 mwaka 2023/24, kabla ya kufikia shilingi bilioni 7.55 mwaka 2024/25, hatua inayoonesha ukuaji mkubwa wa sekta hiyo na mchango wake katika uchumi wa taifa.

Naye Fundi Sanifu Madini kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Mtwara, Nurah Juma, amesema madini ya ujenzi kama mawe na kokoto yanayochimbwa katika kijiji cha Chipite wilayani Masasi yameendelea kuwa mhimili muhimu wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika mikoa ya Mtwara na Lindi.

Amesema kokoto zinazozalishwa katika eneo hilo zinatumika katika ujenzi wa barabara, majengo, upanuzi wa Bandari ya Mtwara na viwanja vya ndege, pamoja na ujenzi wa Bandari mpya ya Kisiwa Mgao, hali inayochangia upatikanaji wa vifaa vya ujenzi vyenye ubora na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika ukanda wa kusini.









Top News