NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara, Deniss Londo, amesema kupitia Shirika la Utafiti na Maendeleo ya Viwanda Tanzania (TIRDO),vijana wabunifu wanapata fursa ya kubadili mawazo yao ya kiteknolojia na ujasiriamali kuwa bidhaa na huduma zenye tija katika soko.

Amesema viwanda vina mchango mkubwa katika utoaji wa ajira, kuimarisha usalama wa kiuchumi na kukuza ubunifu, hususan kwa vijana.

Ameyasema hayo leo Januari 23, 2026 Jijini Dar es Salaam alipotembelea ofisi za TIRDO ambapo amefurahishwa na shughuli inayofanywa na shirika hilo hasa utafiti kwenye maendeleo ya viwanda nchini.

Amesema kuwa jukumu la TIRDO si kuanzisha viwanda moja kwa moja, bali ni kufanya utafiti, kusambaza teknolojia na kusaidia wazalishaji wadogo na wa kati kupunguza gharama za uzalishaji na kuongeza tija.

Aidha amewapongeza viongozi na wataalamu wa TIRDO kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kulea wajasiriamali waliotoka ngazi ya chini hadi kufikia uzalishaji wa viwandani ambapo kuvutiwa na miradi ya urejelezaji wa taka za plastiki pamoja na matumizi ya teknolojia rafiki kwa mazingira, akisema miradi hiyo inalinda mazingira na wakati huo huo kuleta ajira kwa wananchi.

Hata hivyo amesema kuwa ushirikiano kati ya wizara, taasisi za umma na mamlaka za serikali za mitaa ni muhimu ili kuhakikisha miradi ya viwanda inatekelezwa kwa kuzingatia sera, viwango na mahitaji halisi ya wananchi. Ameahidi kuyafikisha mapendekezo ya wadau katika ngazi ya wizara kwa lengo la kuyaendeleza katika maeneo mbalimbali nchini.

Pamoja na hayo amesema kuwa maendeleo ya viwanda bado ni nguzo kuu ya ukombozi wa kiuchumi wa Tanzania, akisisitiza kuwa bila uwekezaji wa kimkakati katika sekta ya viwanda, taifa haliwezi kufikia maendeleo endelevu.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TIRDO, Prof. Mkumbukwa Mtambo, amesema kuwa wanatarajia kuanzisha kituo cha kutengeneza na kufanyia matengenezo vifaa vya kielektroniki kwa ajili ya kukuza ubunifu wa ndani na kupunguza utegemezi wa teknolojia kutoka nje.



















Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Mhe. Edward Mpogolo, amefanikiwa kumaliza mgomo wa wafanyakazi zaidi ya 1,500 wa Kiwanda cha NAMERA kilichopo Gongolamboto, jijini Dar es Salaam, mgomo uliokuwa umeanza tarehe 16 Januari, 2026.

Mgomo huo ulitokana na madai ya mishahara, ambapo mshahara wa kima cha chini kwa sekta binafsi umewekwa kwa mujibu wa Tangazo na Amri ya Serikali Namba 605A ya tarehe 13 Oktoba, 2025, inayotoa ongezeko la wastani wa asilimia 33.4. 

Kutokana na ongezeko hilo, mshahara wa chini umeongezeka kutoka Shilingi 275,060 mwaka 2022 hadi Shilingi 358,222 mwaka 2025. Hivyo basi, hakuna mtu au taasisi yoyote inayoruhusiwa kulipa mshahara chini ya kiwango kilichobainishwa katika Amri hiyo ya Serikali, hata kwa kuwepo kwa makubaliano yoyote kati ya taasisi binafsi kupitia chama chao cha waajiri (ATE) au mifumo mingine ya ndani.
Akizungumza na wafanyakazi pamoja na uongozi wa kiwanda hicho, Mhe. Mpogolo amesisitiza kuwa Amri ya Serikali ni ya lazima kutekelezwa na kwamba hakuna kampuni, taasisi au mwajiri yeyote anayekubalika kushuka chini ya viwango vilivyowekwa kisheria. Ameeleza kuwa makubaliano yoyote hayawezi kwenda kinyume na Amri ya Serikali.
Mpogolo ametoa maelekezo muhimu kwa uongozi wa kiwanda na wafanyakazi, ikiwemo kuhakikisha malipo ya mishahara yanatolewa kwa mujibu wa Tangazo la Serikali Na. 605A la mwaka 2025, huku akisisitiza kuwa hakuna mfanyakazi atakayefukuzwa kutokana na kushiriki mgomo, ili kuimarisha mahusiano bora kati ya mwajiri na waajiriwa. 

Aidha, ameitaka kiwanda kushirikiana na Chama cha Wafanyakazi (TUICO) na Afisa Kazi wa Mkoa wa Dar es Salaam kufanyika uchaguzi wa viongozi wa wafanyakazi watakao kuwa kiungo madhubuti kati ya wafanyakazi na uongozi, pamoja na kupitia mikataba ya ajira kuhakikisha inakidhi sheria na kanuni zinazohitajika. Mpogolo pia amehimiza ujenzi wa mahusiano mazuri na kulinda kiwanda kutokana na mchango wake mkubwa katika uchumi wa taifa na nafasi zake muhimu za ajira kwa wananchi.

Kwa upande wao, wafanyakazi wa kiwanda hicho wameeleza kuridhishwa na hatua zilizochukuliwa na Mkuu wa Wilaya, wakisema kuwa zimeleta matumain

 


Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Dennis Londo amelipongeza Shirika la Maendeleo ya Viwanda Vidogo (SIDO) kwa kutekeleza ahadi ya siku 100 ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kutoa mikopo ya zaidi ya shilingi bilioni moja kwa wajasiriamali ili kuendeleza miradi mbalimbali ya viwanda nchini.

Amebainisha hayo Januari 23, 2026, alipofanya ziara ya kikazi katika shirika hilo na kuipongeza menejimenti kwa kasi ya kuridhisha ya utekelezaji wa maelekezo ya serikali.

Mhe. Londo amesisitiza kuwa viwanda vidogo ni moyo wa uchumi endelevu kwani vinamsaidia mwananchi hasa vijana kupata ajira na kuleta maendelwo kuanzia ngazi ya familia na kuchochea uingizaji wa fedha za kigeni.

Amesema kupitia SIDO, bidhaa za Kitanzania zinaweza kuteka soko kubwa la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), jambo litakaloinua hadhi ya viwanda vya ndani katika medani za kimataifa.

Kufuatia ziara hiyo, Naibu Waziri ameiagiza SIDO kuangalia namna ya kuongeza kutoa ruzuku (grants) kwa vijana ili kuhakikisha wanawekeza kwa kutumia rasilimali zilizopo bila kukwama, lengo ni kuhakikisha kuwa ukosefu wa mtaji haubaki kuwa kikwazo kwa vijana wabunifu wanaotaka kuingia katika sekta ya uzalishaji na viwanda.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Sera na Mipango, Bw. Audax Bahweitima, amesema Sera ya Maendeleo ya Wajasiriamali Wadogo na wa Kati (SMEs) inalenga kuboresha miundombinu ya biashara na teknolojia na kusisitiza kuwa SIDO ndiye mtekelezaji mkuu wa sera hiyo kwa kuhakikisha upatikanaji wa fedha na zana za kisasa za uzalishaji unawafikia walengwa kwa wakati.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa SIDO, Mhandisi Prof. Sylvester Mpanduji, amesema kuwa hadi sasa wanufaika 196 wamefikiwa na mikopo hiyo, na kufanikiwa kuzalisha jumla ya ajira 546. Takwimu hizo zinaonyesha mafanikio makubwa kwa kundi la vijana, ambao wamechukua nafasi 436 kati ya ajira hizo mpya zilizotengenezwa.

Aidha, Prof. Mpanduji ameongeza kuwa kupitia ushirikiano na Shirika la Kimataifa la Wahamiaji (IOM), wametoa ruzuku ya shilingi milioni 51 kwa vijana tisa ili kukuza viwanda vyao.














Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) imesema itaendelea kutumia tasnia ya sekta ya michezo ili kujenga mahusiano ya undugu, ujamaa, umoja na mshikamano wa Watanzania ili kuenzi misingi ya Muungano.

Rai hiyo imetolewa leo Ijumaa (Januari 23, 2026) na Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo, Dkt. Richard Muyungi wakati wa ziara yake ya kutembelea kambi ya timu ya Netiboli ya Ofisi hiyo inayoshiriki mashindano ya Ligi ya Muungano wa netiboli inayoendelea katika Uwanja wa Amani Complex, Zanzibar.

Dkt. Muyungi amesema michezo ni sekta muhimu inayotumika katika kujenga mashirikiano na uhusiano katika jamii na hivyo Ofisi hiyo itaendeleza jitihada mbalimbali katika kuhakikisha michezo itakuwa sehemu muhimu katika kuimarisha Muungano.

“Nia na malengo ya waasisi wetu wakati wanaanzia Muungano ni Pamoja na kuhakikisha wanatumia fursa mbalimbali ikiwemo michezo ili kuweza kujenga mahusiano ya undugu, familia na fursa nyingine za kijamii na kiuchumi” amesema Dkt. Muyungi.

Ameeleza kuwa kupitia sekta ya michezo hususani mashindano ya Ligi ya Netiboli, Ofisi hiyo imeweza kutangaza vyema Muungano ambapo wachezaji wa timu wameweza kuwa kucheza kwa juhudi kubwa na kuibuka kwa matokeo ya ushindi katika michezo yake.

Aidha mbali na ziara hiyo Dkt. Muyungi pia alikabidhi zawadi ya pesa taslimu Shilingi 500,000/- kwa kila mchezaji wa timu hiyo ikiwa ni sehemu ya motisha kwa wachezaji hai ili kuwaongezea morali ya kupata matokeo ya ushindi katika michezo yake iliyosalia.

“Nimetoa zawadi hii ya pesa kama motisha kwenu kwa ajili ya kufanya vizuri zaidi, niseme tu yajayo yanafurahisha…tuongeze juhudi katika michezo iliyosalia ili tuweze kuchukua ubngwa wa mashindano haya” amesema Dkt. Muyungi.

Kwa upande wake Kocha wa Timu wa hiyo, Mafuru Buriro amesema menejimenti ya Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kwa kuiwezesha timu kupata mahitaji yote ya msingi hatua iliyowezesha kuwa na kambi nzuri iliyojiandaa vyema kwa ajili ya mashindano hayo.

“Tunamshukuru sana Katibu Mkuu kwa kuwa karibu na timu tangu mwanzo wa mashindano haya kwani hiyo ndiyo iliyokuwa siri ya mafanikio ya ushindi wat imu katika michezo yote tuliyocheza” amesema Buriro.

Amesema timu hiyo imecheza jumla ya michezo 10 ambapo imeshinda michezo 9 na kupoteza mchezo dhidi ya timu ya Kikosi cha Valantia Zanzibar (KVZ) amba oni mabingwa watetezi wa mashindano hayo.

Kwa upande Katibu wa Klabu ya Michezo Ofisi ya Makamu wa Rais, Marwa Nyaisawa amesema mashindano ya Ligi ya Muungano ya Netiboli ni moja ya mashindano mahsusi katika kuonesha umma kuwa Ofisi hiyo imejiandaa vyema kwa ajili ya kuonesha ushindani katika michezo mbalimbali.

Naye mchezaji wa timu hiyo, Bi. Habiba Mhina ameishukuru Menejimenti ya Ofisi hiyo kwa kutoa nafasi kwa watumishi wanawake kuweza kushiriki maonesho hayo kwani yameweza kwani mbali na kuimarisha afya michezo hiyo pia imeweza kuwakutanisha na wadau mbalimbali.

Mashindano ya Ligi ya Muungano ya Netiboli mwaka 2026, yalishirikisha jumla 11 ikiwemo timu sita (06) kutoka Tanzania Bara na timu tano (05) kutoka Zanzibar.









Top News