WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, ameshiriki ibada ya Jumapili, leo, tarehe 11 Januari 2026, katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Mashariki na Pwani (DMP), Usharika wa Azania Front, jijini Dar es Salaam.

Ibada hiyo iliongozwa na Msaidizi wa Askofu wa KKKT DMP, Chediel Lwiza, kwa kushirikiana na mchungaji Victor Makundi. 






Naibu waziri wa maji Eng.Kundo Mathew amemuelekeza katibu mkuu wizara ya maji Kumfatilia mkandarasi aliyekabidhiwa mradi wa kuondosha maji taka uliopo katika kata ya Katende halmashauri ya wilaya ya Chato mkoani Geita na kuhakikisha anaondolewa kabisa katika mikataba ya wizara hiyo.

Ni wakati alipotembelea ujenzi wa mradi wa kuondosha maji taka na kukuta umetelekezwa na mkandarasi huyo ambaye hakuepo eneo la kazi.

Mradi wa kuondosha maji taka katika wilaya ya chato unaghalimu kiasi cha takribani shilingi bilioni 1.5 ambapo mpaka sasa mkandarasi ameshakabidhiwa takribani shilingi milioni 800 na kuutelekeza mradi huo.

Wilaya ya chato ina uhitaji mkubwa na mradi huo hususani kipindi cha mvua kutokana na kusambaa kwa maji taka katika maeneo mengi hivyo kuwaibua viongozi katika wilaya hiyo kumuangukia naibu waziri juu ya kukamilika kwa mradi huo.

Diwani wa kata ya Bungila Batromeo Christian amesema kuwa mradi huo ulinzishwa mnamo mwaka 2022 lakini mpaka sasa bado unasuasua huku mkandarasi akiwa ameshakula fedha nyingi.






NA EMMANUEL MBATILO, MICHUZI TV

Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imekabidhi jumla ya vitabu vya Elimu ya Dini ya Kiislamu kwa Taasisi ya Kusimamia Ufundishaji wa Elimu ya Dini ya Kiislamu (TISTA), ikiwa ni hatua ya kuimarisha ufundishaji wa somo hilo katika shule za sekondari nchini.

Makabidhiano hayo yamefanyika leo Januari 11, 2026 katika Ofisi za Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) jijini Dar es Salaam, ambapo Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Mhe. Abubakar Zuberi, ameupokea mzigo huo wa vitabu kwa niaba ya TISTA akiongozana na viongozi wengine wa taasisi hiyo.

Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Prof. Adolf Mkenda, amesema wamekabidhi nakala 5,000 za vitabu vya kiada vya somo la Elimu ya Dini ya Kiislamu kwa kidato cha pili vyenye thamani ya shilingi milioni 16, pamoja na nakala 1,000 za vitabu vya mwongozo wa mwalimu vyenye thamani ya shilingi milioni 1.2, na kufanya jumla ya vitabu vyenye thamani ya shilingi milioni 17.2.

Prof. Mkenda ameongeza kuwa Serikali itaendelea kuchapa na kusambaza vitabu vya Elimu ya Dini ya Kiislamu kwa kidato cha sita pamoja na vile vya kidato cha tatu na cha nne mara tu vitakapokamilika, na kuzipa nakala kadhaa BAKWATA kwa ajili ya kusambaza katika shule zisizo za Serikali Tanzania Bara na Zanzibar.

Aidha, ametoa shukrani kwa Taasisi ya Elimu Tanzania (TET) kwa kushirikiana kwa karibu na TISTA na kufanikisha zoezi la uandishi pamoja na uidhinishaji wa vitabu hivyo.

Amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na madhehebu yote ya dini ili kuhakikisha Elimu ya Dini inafundishwa ipasavyo na kuchangia katika kujenga Mtanzania mwenye maadili mema.

Kwa upande wake, Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Mhe. Abubakar Zuberi, ameishukuru Serikali kwa ushirikiano uliowezesha uandaaji wa maudhui ya vitabu vya Elimu ya Dini ya Kiislamu, akieleza kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kuimarisha malezi na maadili kwa wanafunzi nchini.














Na Mwandishi Wetu

PEMBA

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni amesema Pemba ina vivutio vingi vya utalii hivyo ujenzi wa Bandari yaMkoani, Pemba itafungua zaidi milango katika sekta mbalimbali.

Mhe. Masauni amesema, Bandari ya Mkoani ni kiunganishi na muhimili wa maisha ya kila siku ya wananchi wa Pemba, ni lango la biashara, elimu, afya, utalii na mshikamano wa kijamii katiya Pemba, Unguja na Tanzania Bara.

Ameyasema hayo Januari 10, 2026 wakati akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa jengo jipya la kisasa la abiria katika bandari hiyo ambapo jengo hilo litakuwa na uwezo wa kuhudumia abiriazaidi ya 1,500 na kuinua huduma za bandari kwa viwango vya kimataifa, ikiwa ni shamrasharakuelekea miaka 62 ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Amesema takwimu zinaonesha kuwa zaidi ya asilimia 90 ya abiria wanaosafiri kwenda nakutoka Kisiwa cha Pemba hutumia usafiri wa baharini, hali inayoifanya bandari hiyo kuwa naumuhimu kwa ajili ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

“Usafiri wa baharini si mbadala, bali ni mahitaji muhimu ya maisha ya wananchi wetu, ndiyomaana Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imeona umuhimu wa kuwekeza katika miundombinu yakisasa, salama kwa abiria,” amesema Mhe. Masauni.

Amesema ujenzi wa jengo hilo unatokana na mkataba wa uwekezaji kati ya Shirika la Bandari nawawekezaji wa Fumba Port, akibainisha kuwa ni mfano mzuri wa ushirikiano kati ya Serikali nasekta binafsi katika kuharakisha maendeleo ya miundombinu ya kimkakati.

“Ushirikiano huu unapunguza mzigo kwa Serikali, unaongeza ubora na ufanisi wa huduma, nakuchochea uchumi kupitia ajira kwa vijana na wananchi kwa ujumla,” amesema.

Amewata watoa huduma wa bandari, waendeshaji wa vyombo vya usafiri wa majini pamoja naabiria kuitumia miundombinu hiyo kwa nidhamu, uadilifu na kuitunza ili idumu kwa mudamrefu kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo, wakandarasi na wasimamizi wa mradikuhakikisha ujenzi unatekelezwa kwa ubora unaostahili, kwa wakati na kwa kuzingatia thamaniya fedha.

Naye, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Bandari Zanzibar, Akif Ali Khamis, amesemakukamilika kwa mradi huo kutasaidia kwa kiasi kikubwa kukabiliana na changamoto yaupatikanaji wa usafiri wa uhakika kwa abiria wanaosafiri kati ya Pemba, Unguja na Tanzania Bara.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Mkoani, Pemba Mhe. Miza Hassan Faki, amesemauwepo wa bandari hiyo umechangia ongezeko la meli zinazotia nanga katika eneo hilo, akisemakuwa awali bandari ilikuwa inapokea abiria 60,000 kwa mwezi lakini kwa sasa inapokea zaidi yaabiria 100,000.

Ameongeza kuwa bandari hiyo imechangia pia kuongeza ajira kwa wananchi wa maeneo yajirani, hususan vijana ikiwa pamoja na kupunguza changamoto ya upatikanaji wa mafuta ambapoawali uwezo wa kuhifadhi mafuta ulikuwa lita 100,000, lakini kwa sasa umeongezeka hadikufikia lita milioni mbili.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa jengo jipya la kisasa la abiria katika Bandari ya Mkoani, Mkoa wa Kusini Pemba, Januari 10, 2026.


Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni (wa kwanza kushoto) akimsikiliza Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Bandari Zanzibar, Akif Ali Khamis kabla ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa jengo jipya la kisasa la abiria katika Bandari ya Mkoani, Mkoa wa Kusini Pemba, Januari 10, 2026.
 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni akizungumza na wananchi mara baada ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa jengo jipya la kisasa la abiria katika Bandari ya Mkoani, Mkoa wa Kusini Pemba, Januari 10, 2026.

PICHA NA OFISI YA MAKAMU WA RAIS

Na Mwandishi Wetu, Karatu.

NAIBU Waziri wa Ofisi ya Rais-Utumishi, Regina Qwaray, ameonyesha kuridhishwa na utekelezaji wa miradi iliyojengwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii ( TASAF) kupitia mradi wa OPEC,ikiwemo wa ujenzi wa Shule mpya ya Sekondari ya Laja,wilayani Karatu.

Ametoa pongezi hizo jana wilayani humo alipotembelea Shule hiyo iliyojengwa katika Kijiji cha Laja,Karatu mkoani Arusha ikiwa ni mwendelezo wa ziara zake mkoani humo.

Amesema ujenzi wa shule hiyo umeleta matokeo mazuri kwa jamii ikiwemo kuondoa adha ya wanafunzi waliokuwa wakitembea umbali mrefu kutokana na kijiji hicho kutokuwa na shule.

"Wanafunzi wengi walikuwa hawafiki shule,wengi walikuwa watoro lakini kupitia mradi huu ambapo hadi mabweni yamejengwa umesaidia kuondoa changamoto hiyo,"amesema

"Niwapongeze wananchi kwa kujitoa kwenu na kuona thamani ya elimu kwani mmeshiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo na kuchangia mradi huu,tutunze mradi huu,"

Pia amewataka wazazi kutambua umuhimu wa kusomesha watoto na kuwa elimu ni hazina kwa vijana na inasaidia kuongeza wasomi na kuongeza kasi ya mabadiliko.

Awali Kaimu Mratibu wa TASAF Wilaya ya Karatu, Athanasi Sarwatt,amesema mradi wa ujenzi wa Shule mpya ya Sekondari Laja umegharimu zaidi ya Sh.milioni 774.9 ambapo TASAF kupitia OPEC awamu ya nne walitoa Sh.milioni 659.5 huku zaidi ya Sh.milioni 115 zikiwa ni michango ya wananchi ikiwemo mchanga,kokoto,mawe,maji na nguvu kazi.

Amesema mradi huo umesaidia kuondoa utoro kwa wanafunzi kwani awali walikuwa wanasafiri umbali mrefu zaidi ya kilomita nane kwenda shule na kuwa mpango umesaidia kuongeza mahudhurio ya wanafunzi shuleni hasa wanaotoka kaya maskini sana.

Amesema shule hiyo ilisajiliwa Novemba 2023 na kuanza rasmi mwaka 2024 kwa kupokea wanafunzi 26 wa kidato cha kwanza na kwa sasa shule ina jumla ya wanafunzi 63 ambao ni kidato cha kwanza na pili na wote wanakaa bweni.

Kwa upande wake Mratibu wa TASAF mkoa wa Arusha,Richard Nkini,amesema kwa kipindi cha miaka miwili mkoa huo umepokea zaidi ya Sh 23 Bilioni kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ambayo imeleta tija na mabadiliko katika jamii.

Wakati huo huo Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Karatu, Juma Hokororo, ameshukuru TASAF kwa utekelezaji wa miradi mbalimbali hasa ya elimu na kuwa imesaidia kuinua elimu.

Amesema katika kipindi ambacho Shule zinakaribia kufunguliwa,halmashauri hiyo imeweka mikakati kuhakikisha watoto wote ambao wana umri wa kwenda shule wanaandikishwa  na kuripoti shule pamoja na wale waliofaulu wanaotakiwa kujiunga Kidato cha kwanza.










 Na Mwandishi wetu.

Tanzania imeendelea kung’ara kimataifa baada ya Benki ya Dunia (World Bank - WB) kuitaja kuwa miongoni mwa nchi zilizo na ukomavu wa juu wa matumizi ya TEHAMA katika sekta ya umma, hatua inayothibitisha mafanikio ya mageuzi ya kidijitali yanayoendelea kutekelezwa na Serikali.

Kwa mujibu wa Ripoti ya Ukomavu wa Matumizi ya Teknolojia Duniani katika Utoaji wa Huduma za Serikali na Ushirikishwaji wa Wananchi  ‘GovTech Maturity Index - GTMI’ ya Benki ya Dunia mwaka 2025, Tanzania imeorodheshwa katika Kundi A - Ukomavu wa Juu wa matumizi ya TEHAMA (Extensive GovTech Maturity), kundi linalojumuisha nchi zinazoongoza duniani katika matumizi ya teknolojia katika kuboresha utoaji wa huduma za serikali na ushirikishwaji wa wananchi. 

Ripoti hiyo hutathmini kiwango cha ukomavu wa TEHAMA serikalini takriban katika nchi zote duniani, kwa kuzingatia maeneo mbalimbali yakiwemo sera, sheria, miongozo, mifumo, na utekelezaji wake ambapo, katika mwaka uliopita ripoti hiyo ilitolewa mwezi Desemba, 2025. 

Hii ni mara ya pili kwa Tanzania kutambuliwa na Benki ya Dunia (WB) katika kupiga hatua ya ukomavu wa TEHAMA, ambapo mwaka 2022 Tanzania ilitajwa kuwa miongoni mwa nchi zilizofanya vizuri zaidi duniani katika GovTech Maturity Index. Katika utafiti huo uliohusisha nchi 198, Tanzania ilipanda kutoka nafasi ya 90 mwaka 2021 hadi nafasi ya 26 mwaka 2022 na kutoka kundi B hadi kundi A. Barani Afrika, Tanzania ilishika nafasi ya pili baada ya Mauritius na kuwa kinara wa ukanda wa Afrika Mashariki.

Kuimarika kwa Nafasi ya Tanzania Kimataifa

Mafanikio haya ni mwendelezo wa safari ya Tanzania ya kupanda ngazi katika ukomavu wa TEHAMA serikalini, na kuendelea kujijengea taswira chanya kimataifa na kikanda.

 Tanzania imeendelea kuonesha uthabiti katika matumizi ya teknolojia kama nyenzo ya kuboresha ufanisi wa taasisi za umma, kuongeza uwazi na kuimarisha uwajibikaji katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

Kwa upande wa bara la Afrika, Tanzania imeendelea kuwa miongoni mwa nchi vinara wa mageuzi ya kidijitali serikalini, ikilinganishwa na mataifa mengine yaliyofanyiwa tathmini katika ripoti hiyo. Tanzania ni moja kati ya nchi  tano tu katika bara la Afrika ambazo zimeingia kwenye kundi la juu la ukomavu wa TEHAMA Serikalini, nchi nyingine ni Kenya, Misri, Uganda na Rwanda. 

Ripoti ya GovTech Maturity Index (GTMI) 2025 imeangazia maeneo  makuu manne ya TEHAMA:

Mifumo ya Mikuu ya Serikali (Core Government Systems)

Huduma Zinazotolewa Mtandaoni  (Online Public Service Delivery)

Jukwaa la Ushirikishwaji Wananchi Kidijitali (Digital Citizen Engagement) 

Mazingira Wezeshi (GovTech Enablers).  

Mifumo ya Mikuu ya Serikali Yachochea Mafanikio

Ripoti ya Benki ya Dunia inaonesha kuwa, mafanikio ya Tanzania yametokana kwa kiasi kikubwa na uwepo na matumizi ya Mifumo ya Mikuu ya Serikali (Core Government Systems).

 Mifumo hiyo imejumuisha mifumo ya usimamizi wa rasilimaliwatu kama vile (Mfumo wa Taarifa za Watumishi na Mishahara - ‘Human Capital Information Management System’  - HCIMS’), mifumo ya ajira (Ajira Portal), pamoja na mifumo ya kuunganisha na kubadilishana taarifa kati ya taasisi za umma (interoperability).

Mfumo Mkuu wa Ubadilishanaji Taarifa Serikalini (Government Enterprise Service Bus – GovESB) umetajwa kuwa mhimili muhimu unaowezesha mifumo ya taasisi mbalimbali za umma kusomana na kubadilishana taarifa kwa usalama na ufanisi zaidi. Hatua hii imepunguza urudufu wa taarifa, kuharakisha utoaji wa huduma na kuongeza uwajibikaji.

Ushirikishwaji wa Wananchi Kidijitali Katika eneo la Ushirikishwaji wa Wananchi Kidijitali (Digital Citizen Engagement), Tanzania imetajwa kuwa miongoni mwa nchi zinazochukua hatua madhubuti katika kujenga mifumo inayowawezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika masuala ya utawala.

Mfumo wa e-Mrejesho umekuwa ni nyenzo muhimu inayowaunganisha wananchi na Serikali, kwa kuwezesha utoaji wa maoni, malalamiko, ushauri na pongezi, pamoja na kupata mrejesho kwa wakati. Mfumo huu umechangia kuimarisha uwazi, uwajibikaji na imani ya wananchi kwa Serikali.

Mazingira Wezeshi (GovTech Enablers)

Ripoti hiyo pia inaonesha kuwa Sera, Sheria, Kanuni, Viwango na Miongozo ya Serikali Mtandao (GovTech Enablers) vimekuwa chachu ya mafanikio ya Tanzania katika mageuzi ya kidijitali. Mazingira haya rafiki yameiwezesha Serikali kuwekeza na kusimamia miradi ya TEHAMA kwa mwelekeo mmoja wa kitaifa.

Utoaji wa Huduma Mtandaoni (Online Public Service Delivery)

Aidha, utoaji wa huduma za serikali kwa njia ya mtandao (Public Service Delivery) kupitia mifumo mbalimbali ikiwemo Mfumo Mkuu wa Malipo Serikalini (GePG), Mfumo wa Kitaifa wa Manunuzi ya Kielektroniki (NeST) na mifumo ya huduma za Serikali za Mitaa (TAUSI), umeongeza upatikanaji wa huduma kwa wananchi kwa ufanisi na kwa gharama nafuu.

Mtazamo wa e-GA

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA), Mhandisi Benedict Ndomba, amesema kuwa mafanikio hayo ni ushahidi wa mwelekeo sahihi wa taifa katika kujenga Serikali ya kidijitali.

Amesisitiza kuwa, uwepo wa mifumo mbalimbali ya TEHAMA serikalini unaonesha usimamizi mzuri wa rasilimali za TEHAMA, na kutoa wito kwa taasisi za umma kuendelea kuzingatia Sheria, Kanuni, Viwango na Miongozo ya Serikali Mtandao katika utekelezaji wa miradi ya TEHAMA. Pia amehimiza matumizi ya mifumo ya ushirikishwaji wa wananchi na kuunganisha mifumo ya taasisi na GovESB.

Mafanikio haya yanaifanya Tanzania kuwa kielelezo cha mageuzi ya kidijitali barani Afrika, na kuweka msingi imara wa kuendelea kuboresha utoaji wa huduma za umma, kukuza uwazi na kuimarisha uchumi wa kidijitali kwa maendeleo endelevu ya taifa.



*Asema ndio sababu za kumteua Profesa Kabudi kuwa Ofisi ya Rais Ikulu

Na Said Mwishehe,Michuzi TV

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Samia Suluhu Hassan amesema ameteua aliyekuwa Makamu wa Rais Dk.Philip Mpango kuwa Mshauri wake katika uchumi na miradi na aliyekuwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kuwa mshauri wake katika mambo ya jamii.

Hivyo amesema kutokana na kuwa na washauri hao katika ofisi yake ndio maana ameamua kufanya mabadiliko katika Baraza la Mawaziri kwa kumteua aliyekuwa Waziri wa Habari,Utamaduni ,Sanaa na Michezo Profesa Palamagamba Kabudi amemteua kuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais -Kazi Maalum 

Akizungumza leo Januari 10,2026 Ikulu Dar es Salaam katika hafla ya kuwapongeza wanamichezo mbalimbali wakiwemo timu ya Taifa Stars iliyofanikiwa kuingia 16 Bora katika michuano ya AFCON ,Rais Samia ametumia nafasi hiyo kuelezea sababu ya kumteua Profesa Kabudi kuwa Ikulu.

“Pamoja na kwamba leo ni siku ya kuwapongeza wana michezo waliofanya vizuri kama vijana wangu wa Taifa Stars lakini pia shughuli hii imekuwa wakati maalum kumuaga Profesa Kabudi kutoka kwenye michezo na kuja kwangu Ikulu.

“Imekuwa mapema kubadilisha lakini kwasababu kuendana na siasa za dunia zinavyokwenda ambazo zinajicho chanya kwa Tanzania na nyingine jicho hasi kwa Tanzania.

“Pale Ikulu nahitaji akili iliyopevuka yenye maarifa mapana , uzoefu mkubwa na mtu ambaye yuko vizuri kujieleza na anaweza kulieleza jambo likaeleweka hivyo nimepiga picha serikalini kwangu kote nikasema Profesa Kabudi atanifaa

“Lakini jingine ni kwamba punde hivi nimeteua washauri wa Rais.Nimemteua aliyekuwa Makamu wa Rais kuwa mshauri wa uchumi na miradi na nimemteua aliyekuwa Waziri Mkuu atakuwa ananishauri mambo ya jamii.

“Sasa vile vichwa viwili vikubwa vinahitaji mtu aliyetulia mtulivu anayeweza kwenda nao,hawa watoto wangu wanaweza kujijibia tu ikaja kesi lakini Profesa Kabudi anaweza kwenda nao.

“Kwahiyo hiyo ndio sababu nimchukue Profesa Kabudi Ikulu aje anisaidie kazi lakini nikajipa moyo Mwana FA (Hamis Mwinjuma)na Makonda (Paul Makonda)wanaweza kuindesha Wizara ya Michezo vizuri kwasababu ni Wizara ya vijana na wao ni vijana hivyo wataweza ni vijana kwa vijana wenzao

“Ningesema Makonda afanye kazi na washauri wangu wale watu wangesema mama anamjua vizuri Makonda ? Lakini Makonda kwa vijana wenzie yuko vizur sana na Mwana FA kwa wanamistari wenzie yuko vizuri sana,”amesema Rais Samia akitoa sababu za kumteua Profesa Kabudi kwenda Ikulu.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Wanamichezo mbalimbali, Ikulu Jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya kuwapongeza mara baada ya kufanya vizuri katika Mashindano ya Kimataifa, tarehe 10 Januari, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na viongozi mbalimbali kwenye picha ya pamoja na Wachezaji wa Timu ya Taifa ya mpira wa miguu ya Wanaume ya Tanzania ‘Taifa Stars’. Rais Mhe. Dkt. Samia aliwaandalia hafla ya chakula cha mchana na kuwapongeza Wanamichezo waliofanya vizuri Kimataifa, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 10 Januari, 2026. Timu ya Taifa ‘Taifa Stars’ ilishiriki kwenye Kombe la Mataifa ya Afrika ‘AFCON’ nchini Morocco na kufika hatua ya mtoano ambayo ni historia kubwa kwa Tanzania tangu ilipoanza kushiriki michunohiyo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Wanamichezo mbalimbali, Ikulu Jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya kuwapongeza mara baada ya kufanya vizuri katika Mashindano ya Kimataifa, tarehe 10 Januari, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea zawadi ya Jezi ya Timu ya Taifa ya mpira wa miguu ya Wanaume ‘Taifa Strs’ iliyosainiwa na Wachezaji kutoka kwa Nahodha msaidizi wa Timu hiyo, Bakari Nondo Mamnyeto kwenye hafla ya kuwapongeza iliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 10 Januari, 2026.
*Aizungumzia hatua kwa hatua mechi ya Tanzania na Moroco… “Dunia imeona”

Na Said Mwishehe,Michuzi TV

RAIS was Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Samia Suluhu Hassan amewapongeza wachezaji wa Timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ kwa kuipeperusha vema bendara ya Tanzania katika michuano ya AFCON 2025 kwa kufanikiwa kutinga hatua ya 16 bora.

Amesema kiwango kilichooneshwa na Taifa Stars wakati wa mechi ya hatua ya 16 bora dhidi ya Moroco ambao ndio wenyeji wa michuano hiyo dunia imeona Tanzania ilivyopambana na Moroco ametumia nguvu yake kifedha na ushawishi wake kufanya aliyoyafanya katika mchezo ule.

Akizungumza leo Januari 10,2025 Ikulu Dar es Salaam wakati wa hafla ya kuwapongeza wanamichezo mbalimbali na hasa Wachezaji wa Taifa ya Taifa ,Rais Samia amesema anawapongeza kwa dhati kabisa Taifa Stars kwa kufuzu na kufika hatua ya 16 bora ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) kwa mwaka 2025.

“Mafanikio haya ni makubwa na niushahidi soka letu sasa linaendelea kupanda barani Afrika kwa mara ya kwanza nilikaa kwenye televisheni mwanzo mwisho .Siku hiyo nilikuwa nimefunga nikaa kufutari wakati naendelea na futari zangu mchezo (Tanzania na Moroco)unataka kuanza nikaa nikaangalia watoto wangu kazi wanayofanya

“Lakini nimekaa pale nimeangalia mwili wote unauma maana wakipigwa au wakizuiwa mimi eeeehee …wakiwekewa miguu wakisumwa mimi eeee mbona wataniumizia wanangu ,nimeondoka pale mwili unaniuma lakini hongereni mmefanya kazi nzuri sana.

“Na tunajua kwanini yale yalitokea ni kwasababu tunajua tuliocheza nao ni wenyeji, ni taifa lenye fedha , ni taifa ambalo linaushawishi kwa wenzetu hao kwasababu tulikuwa tunaona wazi na Dunia imeona wazi Tanzania ni wapambanaji .Wamepambana lakini lile lililotokea ilikuwa lazıma itokee iwe iwavyo


“Kwahiyo hawawapongeza mmefanya vizuri sana .Nawapongeza pia benchi la ufundi, viongozi wa timu.Ni ukweli michezo yetu imepanda lakini michezo mingine pia imepanda inakwenda juu.


Wakati huo huo Rais Dk.Samia amewapongeza wanamichezo wa timu za Taifa ambapo ameipongeza pia Aidha nizipongeze timu za Taifa niipongeze timu ya Taifa ya Kriketi kwa kushiriki Kombe la Dunia.


“Lakini niipongeze timu ya mpira wa miguu ya watoto wangu wanawake kwa kushiriki Kombe la Dunia nchini Ufilipini hongereni sana.Pongezi pia ziende kwa mabondia wetu waliotwaa makombe ikiwemo timu ya Taifa ya ridhaa iliyopata medali 18 ikiwemo moja ya dhahabu medali za fedha nne na 13 za shaba katika mashindano ya kanda ya tatu ya Afrika yaliyofanyika Nairobi Kenya


“Tunakwenda ndugu zangu tulikotoka sio tuliko leo angalau jina la Tanzania linasikika ,linaonekana kila kwenye fani.Pia niwapongeze kwa ushiriki wa Kombe la Dunia lililofanyika Dubai ambako bondia wetu mmoja alifika hatua ya 16 bora.”


Pia Rais Samia ametoa pongezi kwa timu za Taifa zilizofanya vizuri ukanda wa CECAFA kwa upande wa timu za shule , timu za kuogelea na timu za watu wenye ulemavu zote anazipongeza wamebeba bendera za nchi ya Tanzania.


Ameongeza kwa upande wa ridhaa amempongeza mwanariadhaa Alphonce Simbu kwa kushinda medali ya dhahabu ya Tokhyo marathon 2025 akiwa Mtanzania wa kwanza kutwaa medali ya dhahabu.


“Lakini pamoja naye nimpongeze kijana wetu Cecilia Panga kutwaa dhahabu ya mbio za kilometa 15 zilizofanyika Sao Paulo nchini Brazili kwa kutumia muda wa dakika 51.8 .Hawa ni Watanzania waliopeperusha bendera yetu kwenye riadhaa .


“Nilikuwa namuangalia Simbu akipongezwa anasema amejaribu mara kadhaa lakini safari hii lazıma mimi na medali mara hii lakini akawa na manung’uniko anasema ni jitihada zangu binafsi serikali inamkono kidogo lakini sana binafsi , nikuhakikishie tumeona tutakusapoti huko mbele.


Pamoja na hayo Rais Dk.Samia amesema nidhamu walionesha wanamichezo wote ni alama ya uzalendo na wameipeperusha vema bendera yetu na wameandika historia mpya katika taifa letu na katika ulimwengu wa michezo.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na viongozi mbalimbali kwenye picha ya pamoja na Wachezaji wa Timu ya Taifa ya mpira wa miguu ya Wanaume ya Tanzania ‘Taifa Stars’. Rais Mhe. Dkt. Samia aliwaandalia hafla ya chakula cha mchana na kuwapongeza Wanamichezo waliofanya vizuri Kimataifa, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 10 Januari, 2026. Timu ya Taifa ‘Taifa Stars’ ilishiriki kwenye Kombe la Mataifa ya Afrika ‘AFCON’ nchini Morocco na kufika hatua ya mtoano ambayo ni historia kubwa kwa Tanzania tangu ilipoanza kushiriki michunohiyo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Wanamichezo mbalimbali, Ikulu Jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya kuwapongeza mara baada ya kufanya vizuri katika Mashindano ya Kimataifa, tarehe 10 Januari, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea zawadi ya Jezi ya Timu ya Taifa ya mpira wa miguu ya Wanaume ‘Taifa Strs’ iliyosainiwa na Wachezaji kutoka kwa Nahodha msaidizi wa Timu hiyo, Bakari Nondo Mamnyeto kwenye hafla ya kuwapongeza iliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 10 Januari, 2026.

Top News