Na Mwandishi Wetu, Kigoma

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), Mohamed Salum, amesema mabaharia wana mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi wa taifa kutokana na nafasi yao muhimu katika usafirishaji wa bidhaa zinazoingia na kutoka nchini.

Salum aliyasema hayo wakati akifungua  Warsha  kuelekea kilele cha Maadhomisho  cha Siku ya 16 ya Mabaharia Duniani yanayofanyika mkoani Kigoma, ambapo alieleza kuwa takribani asilimia 80 ya bidhaa zinazoingia nchini husafirishwa kwa njia ya maji na kufikishwa kwa watumiaji kupitia juhudi za mabaharia.

Alisema mchango wa mabaharia hauishii kwenye usafirishaji wa bidhaa pekee, bali pia una athari kubwa katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa kuhakikisha mnyororo wa biashara unaendelea kufanya kazi kwa ufanisi.

“Mabaharia ni nguzo muhimu ya uzalishaji na maendeleo ya uchumi. Bila wao, shughuli nyingi za biashara na usafirishaji zingekwama,” alisema Salum.

Aliongeza kuwa TASAC itaendelea kusimamia na kuratibu sekta ya mabaharia kwa kuhakikisha viwango vya kitaaluma na usalama vinazingatiwa ili mabaharia wa Tanzania waendelee kuwa na ushindani katika soko la ajira duniani.

Akizungumzia changamoto zinazowakabili mabaharia, Salum alisema migogoro inayoendelea katika baadhi ya maeneo duniani, ikiwemo mvutano kati ya Iran na Israel unaohusisha njia muhimu za usafiri wa majini, imeongeza hatari kwa mabaharia wanaotekeleza majukumu yao katika maeneo hayo.

Alibainisha kuwa Tanzania tayari imepoteza mmoja wa mabaharia wake kutokana na changamoto zinazotokana na mazingira ya migogoro, jambo linalosisitiza umuhimu wa kuimarisha ulinzi na usalama wa wafanyakazi hao wanapokuwa kazini.

“Tunahitaji kuona juhudi zaidi za kimataifa katika kulinda mabaharia, kwa sababu wao ndiyo uti wa mgongo wa sekta ya usafirishaji wa majini duniani,” alisema.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa mabaharia kushiriki kikamilifu katika kulinda mazingira ya bahari na maziwa, akieleza kuwa mfumo wa ikolojia wa maeneo hayo una umuhimu mkubwa kwa maisha ya viumbe hai na ustawi wa jamii zinazotegemea rasilimali za maji.

Salum pia alitaja Ziwa Tanganyika kuwa moja ya nyenzo muhimu za uchumi wa Tanzania kutokana na kuunganisha Tanzania na nchi nne jirani, hivyo kutoa fursa kubwa za biashara, usafiri na maendeleo kwa wananchi wa ukanda huo.

Aliwahimiza mabaharia kuendelea kufanya kazi kwa weledi na uzalendo huku akiihakikishia jamii ya mabaharia kuwa Serikali kupitia TASAC itaendelea kuthamini mchango wao, kuimarisha usalama wao na kuboresha mazingira ya kazi ili sekta hiyo iendelee kuwa kichocheo muhimu cha ukuaji wa uchumi wa taifa.

Mkurugenzi Mkuu wa TASAC Mohamed Salum akizungumza wakati akifungua Warsha ya Mabaharia kuelekea Kilele cha Maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani Mjini Kigoma
Mkuu wa Chuo cha DMI Profesa Tumaini Gurumo akizungumza katika Warsha ya Mabaharia katika Maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani mkoani Kigoma.



Matukio katika picha katika Warsha ya Mabaharia mkoani Kigoma

-Zoezi la Uokoaji Kigoma Laonesha Uwekezaji wa Serikali Katika Usalama Majini


Na Mwandishi Wetu, Kigoma

Mkuu wa Wilaya ya Kigoma, Rashid Chuachua, amesema kuwa usalama wa mabaharia na vyombo vya usafiri katika Ziwa Tanganyika ni jambo la msingi linalopaswa kupewa kipaumbele ili ziwa hilo liendelee kuwa nguzo muhimu ya uzalishaji na maendeleo ya uchumi wa Mkoa wa Kigoma na Taifa kwa ujumla.

Chuachua alitoa kauli hiyo wakati wa zoezi la majaribio ya utafutaji na uokoaji lililoshirikisha vikosi vya ulinzi na usalama pamoja na Boti ya Utafutaji na Uokoaji ya Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), lililofanyika katika Bandari ya Kibilizi mkoani Kigoma.

Alisema kuwa kuimarishwa kwa mifumo ya uokoaji na usalama majini kutasaidia kupunguza madhara yanayotokana na ajali za vyombo vya majini, huku akisisitiza umuhimu wa kuongeza ukaguzi wa mara kwa mara wa vyombo hivyo ili kuzuia majanga yanayosababishwa na makosa ya kibinadamu.

“Ziwa Tanganyika ni rasilimali muhimu ya kiuchumi. Ili liendelee kutoa mchango wake kikamilifu, ni lazima tuhakikishe mabaharia na vyombo vya usafiri vinakuwa salama wakati wote,” alisema Chuachua.

Aidha, alisema maadhimisho ya Siku ya Mabaharia pamoja na maonesho ya zoezi la uokoaji yanaonesha dhamira ya Serikali katika kuwekeza kwenye vifaa na miundombinu ya kisasa ya uokoaji kwa lengo la kulinda maisha ya wananchi wanaotumia usafiri wa majini.

Chuachua pia aliwataka mabaharia na waendeshaji wa vyombo vya majini kuhakikisha wanazingatia taarifa za hali ya hewa zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) kabla ya kuanza safari zao ili kujiepusha na hatari zinazoweza kujitokeza kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa.

“Ni muhimu kwa mabaharia kufuatilia utabiri wa hali ya hewa kabla ya kuanza safari. Hii itasaidia kulinda maisha yao pamoja na mizigo inayosafirishwa,” alisisitiza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TASAC, Mohamed Salum, alisema kuwa Boti ya Utafutaji na Uokoaji iliyowekwa katika Ziwa Tanganyika ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuimarisha usalama wa wananchi wanaosafiri kwa njia ya maji na kuhakikisha huduma za uokoaji zinapatikana kwa haraka pale majanga yanapotokea.

Alisema TASAC itaendelea kusimamia viwango vya usalama majini na kutoa huduma bora kwa mabaharia pamoja na wadau wengine wa sekta ya usafiri wa majini nchini.

“Tumeleta boti hii kwa lengo la kuhakikisha wananchi wanaopata majanga majini wanapata msaada wa haraka.Pia tunaendelea kuhimiza mabaharia kutoa taarifa mapema wanapokumbana na changamoto ili hatua za uokoaji ziweze kuchukuliwa kwa wakati,” alisema Salum.

Zoezi hilo limeelezwa kuwa sehemu ya maandalizi ya kuimarisha uwezo wa kukabiliana na dharura majini na kuongeza uelewa wa wadau kuhusu umuhimu wa usalama katika sekta ya usafiri wa majini, hususan katika Ziwa Tanganyika ambalo ni moja ya njia muhimu za usafirishaji na biashara nchini.
Mkuu wa Wilaya ya Kigoma Rashid Chuachua akizungumza wakati zoezi la jaribio la uokoaji lililofanyika katika Bandari ya Kibilizi ikiwa ni maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani yanayoendelea mkoani Kigoma.
Mkurugenzi Mkuu wa TASAC Mohamed Salum akitoa maelezo kuhusiana na zoezi la uokoaji lililofanyika katika Bandari ya Kibilizi katika maadhimisho ya 16 ya Siku Mabaharia Duniani yanayoendelea mkoani Kigoma.
Mkurugenzi wa Usalama wa Usafiri na Mazingira wa Wizara ya Uchukuzi Stella Katondo akizungumza kuhusiana na serikali ilivyowekeza katika uokoaji katika majanga ya usafiri wa majini kwenye maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani yanayoendelea mkoani Kigoma.

Baadhi ya matukio ya jaribio la uokoaji ya mmoja wa afisa aliyejirusha ziwani ili kupata msaada wa kuokolewa.


 

Bodi ya Usimamizi wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) imeanza rasmi utekelezaji wa maagizo yaliyotolewa na Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, ya kuimarisha usimamizi wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala na kuhakikisha changamoto zinazojitokeza katika utekelezaji wake zinatatuliwa bila kurudi kwenye biashara holela ya mazao.

Akitoa taarifa baada ya kutembelea mikoa ya Pwani, Lindi, Mtwara, Ruvuma, Morogoro na Iringa ikiwa ni utekelezaji wa maagizo hayo aliyoyatoa kwenye maadhimisho ya miaka 20 ya Bodi hiyo Mei 19, 2026 jijini Dodoma, Mkurugenzi Mtendaji wa WRRB, Bw. Asangye Bangu, amesema katika ziara hiyo amekutana na viongozi wa mikoa, wilaya na Kamati za Usimamizi wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala na kujionea namna mfumo huo unavyotekelezwa kwenye zao la ufuta.

“Nimeridhishwa na namna serikali za mikoa zinavyoendelea kushirikiana na WRRB katika kuhakikisha mfumo unasimamiwa vizuri. Viongozi wote tuliokutana nao wameonesha utayari mkubwa wa kusimamia utekelezaji wa mfumo huu na kushughulikia changamoto zinazojitokeza,” amesema.

Amesema moja ya maelekezo makubwa yaliyotolewa na Waziri Mkuu ni kuhakikisha changamoto zinazojitokeza katika mfumo huo hazitumiki kama sababu ya kurejea katika biashara holela ya mazao, bali zitafutiwe ufumbuzi kwa wakati.

Kwa mujibu wa Bw. Bangu, changamoto zilizotajwa na Waziri Mkuu zinahusisha miundombinu ikiwamo ujenzi wa maghala, matengenezo ya barabara na uwepo wa mazingira bora ya kurahisisha usafirishaji wa mazao yanayopitia katika mfumo huo. Amesema WRRB imeweka mikakati mahsusi ya kuhakikisha ubora wa mazao unaimarishwa kwa kushirikiana na wakuu wa mikoa na wilaya ili bidhaa zote zinazopelekwa maghalani zikidhi viwango vinavyotakiwa.

“Tumewaelekeza waendesha maghala kuzingatia kikamilifu miongozo iliyotolewa na taasisi husika. Kwa sasa zao lililo sokoni ni ufuta na tayari miongozo ya utekelezaji imetolewa na COPRA,” amesema.

Kuhusu upungufu wa maghala, Bw. Bangu amesema tayari WRRB imeanza mazungumzo na halmashauri mbalimbali ili kuona namna ya kutumia fursa ya uwekezaji katika miundombinu ya maghala ambayo itaongeza ufanisi wa mfumo huo na kuwafikisha wakulima karibu zaidi na minada.

Kadhalika, amesema WRRB kwa kushirikiana na COPRA pia imeanza kuangalia uwezekano wa kuongeza mazao mengine kwenye mfumo ikiwamo karanga, njugu mawe na choroko ili kuongeza idadi ya wanufaika.

Akizungumzia changamoto ya mdororo wa bei, Bangu amesema wananchi wamekuwa wakilinganisha bei za sasa na zile za miaka mitatu iliyopita bila kuzingatia mabadiliko ya soko la dunia, hivyo WRRB imeendelea kutoa elimu kuhusu mwenendo wa bei katika masoko ya kimataifa.

Pia amesema baadhi ya maeneo yamekumbwa na upungufu wa uzalishaji kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa na ukosefu wa mbegu bora, na kwamba WRRB imeanza mazungumzo na Jeshi la Magereza ili kutumia mashamba yake kuongeza uzalishaji wa mbegu.

“Niwahakikishie wananchi kuwa mfumo huu ni imara na tunaendelea kutatua changamoto zote zinazojitokeza. Tukishirikiana na wadau wote, tutamkomboa mkulima wa Tanzania na kuhakikisha anapata thamani halisi ya mazao yake,” alisema.

Na Mwandishi Wetu - Dodoma

SERIKALI imesema imejipanga kikamilifu kukabiliana na madhara yanayoweza kusababishwa na hali ya El Niño kufuatia tahadhari iliyotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA).

Akizungumza hii leo 24 Juni, 2026 wakati wa ufunguzi wa kikao cha wadau wa usimamizi wa maafa, Mkurugenzi Msaidizi Sehemu ya Operesheni na Uratibu kutoka Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) Kanali Selestine Masalamado, amesema kuwa tayari Serikali imeandaa Rasimu ya Mpango wa Taifa wa Dharura ili kuimarisha maandalizi na hatua za kukabiliana na hali hiyo.

Amesema mpango huo unalenga kuhakikisha kunakuwa na uratibu madhubuti, utekelezaji wa hatua za mapema pamoja na kupunguza athari zinazoweza kujitokeza kwa wananchi, mali zao na miundombinu.

“Kikao hiki kinatoa fursa kwa wizara, taasisi, mikoa na wadau wengine kupitia rasimu hii kwa kina na kutoa maoni yatakayosaidia kupatikana kwa mpango shirikishi na unaotekelezeka,” amesema Kanali Masalamado

Ameongeza kuwa Serikali inathamini mchango wa wadau wote katika kuboresha mpango huo ili uwe mwongozo thabiti wa kuzuia, kujiandaa na kukabiliana na madhara ya El Niño.

Aidha, amewataka washiriki kushiriki kikamilifu katika majadiliano na kutoa mapendekezo yenye kujenga yatakayosaidia kulinda maisha ya wananchi na kuhakikisha huduma muhimu zinaendelea kutolewa hata wakati wa majanga.

Katika hatua za maandalizi, amesisitiza umuhimu wa kutoa elimu kwa umma kuhusu tahadhari za kuchukua, ikiwemo kuhama katika maeneo hatarishi na kuendelea na shughuli za kiuchumi katika maeneo salama.

Kwa mujibu wa Kanali Masalamado, kuna umuhimu wa kubaini maeneo salama kwa ajili ya makazi ya muda, pamoja na kuainisha maeneo hatarishi ili kuwezesha hatua za haraka za kukabiliana na maafa.

Sambamba na hilo, amesisitiza kuimarishwa kwa mifumo ya mawasiliano na utoaji wa tahadhari za mapema ili wananchi wapate taarifa sahihi kwa wakati.

“Ninazikumbusha mamlaka za mikoa na serikali za mitaa kuhakikisha kamati za usimamizi wa maafa katika ngazi zote zinatekeleza majukumu yao kikamilifu, huku ufuatiliaji ukiendelea kufanyika mara kwa mara,” amesisitiza

Ameongeza kuwa ni wajibu wa taasisi na mikoa kuhuisha au kuandaa mipango yao ya dharura kwa haraka ili Taifa liwe tayari kukabiliana na athari za El Niño endapo zitajitokeza.

















Na Janeth Raphael MichuziTv

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ametoa wito kwa Watanzania kujenga utamaduni wa kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara ili kuwezesha ugunduzi wa mapema wa saratani, akisisitiza kuwa ugonjwa huo si hukumu ya kifo iwapo utabainika mapema na mgonjwa kupata matibabu stahiki.

Rais Samia ameyasema hayo leo wakati wa uzinduzi rasmi wa Jengo la Tiba ya Mionzi kwa Wagonjwa wa Saratani katika Kilimanjaro Christian Medical Centre mkoani Kilimanjaro Region, ambapo alieleza kuwa Serikali imeendelea kuwekeza katika sekta ya afya kwa lengo la kusogeza huduma muhimu karibu na wananchi.

Akihutubia wananchi, viongozi wa dini na wadau mbalimbali waliohudhuria hafla hiyo, Rais Samia alisema bado kuna haja kubwa ya kuondoa hofu na mitazamo isiyo sahihi kuhusu saratani, huku akisisitiza umuhimu wa uchunguzi wa mapema kama njia bora ya kuongeza nafasi za mafanikio ya matibabu.

“Saratani si hukumu ya kifo. Mtu akigundulika mapema na kufuata maelekezo ya wataalamu wa afya, ana nafasi kubwa ya kupona na kuendelea na maisha yake ya kawaida,” alisema Rais Samia.

Rais huyo alitoa rai maalum kwa wanaume kujitokeza kupima afya zao, hususan uchunguzi wa saratani ya tezi dume, akibainisha kuwa wengi huchelewa kufika hospitalini kutokana na hofu au kuona aibu, jambo linalochangia ugonjwa kugundulika ukiwa umefikia hatua za juu.

“Wanaume wasisite kwenda kupima. Ni muhimu kuchukua hatua mapema kabla ugonjwa haujasababisha madhara makubwa zaidi,” alisisitiza.

Kwa upande wa wanawake, Rais Samia alihimiza uchunguzi wa mara kwa mara wa saratani ya mlango wa kizazi na saratani ya matiti, akieleza kuwa hatua hiyo imekuwa miongoni mwa njia muhimu za kuokoa maisha ya wanawake wengi.

Mbali na wananchi, Rais Samia aliwataka wataalamu wa afya kuongeza juhudi katika utoaji wa elimu kwa umma kuhusu magonjwa yasiyoambukiza, ikiwemo saratani. Pia alipendekeza kuanzishwa kwa siku maalum za uchunguzi wa afya katika jamii ili kuwafikia wananchi wengi zaidi.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Serikali, taasisi za dini, wataalamu wa afya na vyombo vya habari katika kuelimisha umma kuhusu njia sahihi za kinga, uchunguzi na matibabu ya saratani.

Akizungumzia suala la imani na tiba, Rais Samia alisema ni muhimu wananchi kutambua kuwa huduma za afya za kitaalamu zina nafasi muhimu katika kuokoa maisha, huku akihimiza wagonjwa kutotegemea tiba zisizo na uthibitisho wa kisayansi.

“Imani na tiba vinaweza kwenda pamoja. Tunapaswa kutumia maarifa na wataalamu ambao wamewezeshwa kusaidia kuokoa maisha ya wananchi,” alisema.

Ufunguzi wa Jengo la Tiba ya Mionzi katika KCMC unatajwa kuwa hatua muhimu katika kuimarisha huduma za matibabu ya saratani nchini, huku ukitarajiwa kupunguza gharama na safari ndefu kwa wagonjwa waliokuwa wakilazimika kusafiri umbali mrefu kutafuta huduma hizo.

Mradi huo pia unalenga kuongeza upatikanaji wa huduma za kisasa za matibabu ya saratani, kuharakisha uchunguzi na matibabu ya wagonjwa, pamoja na kuboresha kwa ujumla huduma za afya katika ukanda wa Kaskazini mwa Tanzania.






Na Mwandishi wetu,

Serikali itaendelea kushirikiana na Wadau mbalimbali kuhakikisha sanaa na michezo inakuwa sehemu ya ajira na maendeleo kwa Vijana nchini.

Hayo yamebainishwa na Ndugu Emmanuel Shilatu ambaye alikuwa mgeni rasmi kumwakilisha Mkuu wa Wilaya kuzindua mashindano ya Kanda ya Kusini kusaka vipaji vya Sanaa na michezo kwa Watoto.

"Serikali imeweka vipaumbele vyake katika kuendeleza vipawa na vipaji vya Wanafunzi kwa kushirikiana na Wadau mbalimbali wa Michezo. Hivi karibuni Serikali imeboresha mfumo wa elimu kwa ajili ya kuwaandaa Vijana kujifunza amali mbalimbali zikiwepo za michezo na vipaji mbalimbali vya Sanaa." Alisema Shilatu.

Mwandaaji wa Kambi hiyo ya kusaka vipaji ambao ni Shirika la Compassion International amesema jukwaa hilo ni fursa kwa Watoto na Vijana kuonyesha vipaji vyao na kujijengea mustakabali bora huku wakihaidi ubora, haki, nidhamu na burudani ya hali ya juu.

Mmojawapo wa Mzazi ambaye Mwanae anashiriki mashindano hayo Bi. Prisca Richard alionyesha kufurahishwa na Kambi hiyo ya kusaka vipaji vya Michezo kuwa kipaji cha Mwanae anaona kikienda kukua zaidi na ndoto yake kutimia.

Mashindano hayo yameandaliwa na Shirika la Compassion International ambapo yanafanyika Abbey washiriki wakiwa Watu na timu za kutoka mikoa ya kanda ya Kusini ambayo ni Lindi, Mtwara, Ruvuma na Njombe.

Mashindano hayo yanatarajiwa kuhitimishwa tarehe 26 Juni 2026 na yatafungwa na Waziri wa Vijana Mhe. Joel Nnauka.






Na Janeth Raphael MichuziTv

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amezindua rasmi Jengo la Tiba ya Mionzi kwa Wagonjwa wa Saratani katika Kilimanjaro Christian Medical Centre (KCMC), hatua inayotarajiwa kuimarisha huduma za matibabu ya saratani na kupanua upatikanaji wa huduma za kibingwa nchini.

Uzinduzi huo uliofanyika katika hospitali hiyo iliyopo Moshi, Mkoani Kilimanjaro umeelezwa kuwa sehemu ya jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita za kuboresha sekta ya afya kwa kuwekeza katika miundombinu ya kisasa ya matibabu na teknolojia za huduma za kibingwa.

Jengo hilo jipya la tiba ya mionzi linatarajiwa kuongeza uwezo wa KCMC kutoa huduma za kisasa za uchunguzi na matibabu ya saratani, huku likipunguza changamoto ya wagonjwa kusafiri umbali mrefu kufuata huduma hizo katika maeneo mengine ya nchi.

Akizungumza katika hafla hiyo, Rais Samia amesisitiza dhamira ya serikali ya kuendelea kuboresha huduma za afya kwa wananchi kupitia uwekezaji katika vifaa tiba, miundombinu na rasilimali watu, ili kuhakikisha huduma bora zinapatikana karibu na wananchi.

Kukamilika kwa mradi huo kunatajwa kuwa hatua muhimu katika kuimarisha mapambano dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza, hususan saratani, ambayo imeendelea kuwa miongoni mwa changamoto kubwa za afya nchini.

Kwa kuanza kutumika kwa kituo hicho, wagonjwa kutoka Kanda ya Kaskazini na maeneo jirani wanatarajiwa kunufaika na huduma za tiba ya mionzi kwa urahisi zaidi, jambo litakalosaidia kuharakisha upatikanaji wa matibabu na kuongeza matumaini ya uponaji kwa wagonjwa wengi.






Kijana Joseph Mtei mwenye mahitaji maalum ambaye kwa sasa anafanya kazi katika kampuni tangu ya UJUZI katika  kiwanda cha kutengeneza samani cha VETA Dodoma, amepongeza uamuzi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa kumuwezesha kupata ajira rasmi.

Agizo hilo lilitolewa Juni 23, 2026, wakati wa kilele cha wiki ya utumishi wa umma Jijini Dodoma na Waziri wa TAMISEMI, Profesa Riziki Shemdoe, ambaye alimwelekeza Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala bora, kuhakikisha Joseph Mtei anapatiwa ajira rasmi, amesema hatua hiyo imeonyesha kuwa serikali inatambua uwezo wa watu wenye ulemavu na kuthamini mchango wao katika maendeleo ya taifa.

Akizungumza katika mahojiano maalum na Michuzi TV Juni 24, 2026, jijini Dodoma, Mtei alisema safari yake ya maisha imekuwa ya changamoto nyingi tangu utotoni na licha ya kuzaliwa bila mikono lakini hakukata tamaa, Ameeleza kuwa elimu na mafunzo ya ufundi vimemwezesha kujijengea uwezo wa kufanya kazi na kujitegemea kama ilivyo kwa watu wengine wasiokuwa na ulemavu.

Joseph amesema fursa hiyo inapaswa kuwa chachu kwa vijana wengine wenye mahitaji maalum kuendelea kupambana na changamoto zinazowakabili na kutumia fursa zilizopo kujiletea maendeleo, ameeleza kuwa mafanikio yake ni matokeo ya juhudi binafsi, msaada alioupata kwa baadhi ya wadau waliomsapoti kupata elimu pamoja na mazingira yaliyomruhusu kuonyesha uwezo wake kazini.

Aidha, ametoa wito kwa wazazi na jamii kuacha kuwaficha watoto wenye ulemavu na badala yake kuwapa nafasi ya kusoma, kujifunza na kushiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii na kiuchumi, amesema kwa sasa anaishi maisha ya kujitegemea, analipa kodi, anamsomesha mdogo wake, jambo linalothibitisha kuwa ulemavu si kikwazo cha mafanikio.




Na Victor Masangu, Pwani


Serikali ya awamu ya sita katika kupambana na changamoto ya ukosefu wa ajira imeamua kuja na mpango kabambe wa kuanzisha shindano linalojulikana kwa jina la Vijana uchumi Challenge lenye lengo la kuwakutanisha vijana mbali mbali ili waweze kutoa kutoa mawazo yenye kuleta tija katika kuisaidia serikali katika nyanja mbali mbali ikiwemo uchumi na maendeleo.

Hayo yamebainishwa na Naibu Katibu Ofisi ya Rais maendeleo ya vijana Dkt. Kedmon Mapana wakati wa halfa ya uzinduzi rasmi wa kambi maalumu kwa ajili ya usahili wa vijana wapatao 100 bora ambao wamepata fursa ya kuchaguliwa kati ya vijana elfu 7852 walioshiriki hapo awali kutoka mikoa mbali mbali ipatayo 27 ya Tanzania bara na visiwani.

Pia amebainisha kwamba ana imani vijana hao 100 ambao wamechaguliwa na kuweka kambi wataweza kuleta matokeo chanya na kwamba serikali itaendelea kushirikiana nao bega kwa bega na kuchukua mawazo yao ambayo watakwenda kuyafanyia kazi na kuyaendeleza katika maeneo mbali mbali.

"Sisi kama serikali tumeona ni muhimu sana kuwashirikisha vijana wetu wa Tanzania ambao ndio Taifa letu la kesho katika shindano hili ili waweze na wao kuchangia mawazo yao mbali mbali ambayo yataweza kuketa tija zaidi katika kuisaidia serikali katika nyanja mbali mbali za kiuchumi na mambo mengine ya kimaendeleo na mimi nashukuiru sana vijana hao 100 kwa kujitokeza kwa wingi,"amesema Naibu Katibu huyo.

Kadhalika amesema kwamba baada ya kambi hiyo ya vijana watachaguliwa kutoka 100 hadi kufikia vijana 10 ambao watakwenda katika shindano la fainali litakalofanyika mwezi ujao tarehe 6 na kwamba mshindi wa kwamba atajinyakulia shilingi milioni 50, mshindi wa pili milioni 30 na mshindi wa tatu milioni 20 na wengine waliobaki watapewa kifuta jasho.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa kamati ya Kitaifa ya shindano hilo la vijana Uchumi Challenge Joseph Malekele amesema kwamba washirki hao wataweka kambi kwa kipindi cha muda wa siku nne katika katika shule ya Uongozi Mwalimu Julias Nyerere iliyopo Wilaya ya Kibaha Mkoa wa Pwani ambapo pia watapatiwa mafunzo kutoka kwa jopo la majaji mbali mbali.

Mwenyekiti huyo amesema kwamba lengo kubwa la kuandaa shindano hilo ni kuweza kupata mawazo bunifu kutoka kwa vijana ambayo yanaweza kutekelezeka na kuchangia kwa kiasi kikubwa masuala mazima ya kukuza uchumi pamoja na kuweka misingi endelevu katika maendeleo katika sekta mbali mbali za kilimo, usafirishaji, biashara na mambo mengineyo.

Nao baadhi wa vijana hao ambao wamepata fursa ya kuingia katika kambi hiyo akiwemo Raiani Amour na Adrian Thomas wamebainisha kwamba wana imani mawazo na ubunifu wao utaweza kwenda kuleta matokeo chanyaa katika kuwasaidia vijana hasa ambao wamekuwa na changamoto katika ukosefu wa ajira.

Aidha wameipongeza kwa dhati serikali ya awamu ya sita kwa kushirikiana na Wizara ya vijana kwa kuweza kuona umuhimu mkubwa wa kuwakutanisha vijana kutoka maeneo mbali mbali kwa ajili ya kutoa mawazo yao mbali mbali ili kuweza kuisaidia serikali katika mambo mbali mbali.

Kilele cha Shindano hilo la Vijana Challenge kwa mwaka wa 2026 linatarajiwa kufanyika tarehe 6 ya mwezi ujao Jijini Dar es Salaam ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Rais Dkt, Samia Suluhu Hassan.








NA MWANDISHI WETU, DODOMA

Wanawake, vijana na wenye mahitaji maalum sasa wamefikiwa na bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027, kufuatia bajeti hiyo kuongeza asilimia za mikopo ya makundi hayo kutoka asilimia kumi hadi 15.

Akizungumzia suala hilo, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa na Mbunge wa Viti Maalum wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mary Chatanda, Juni 23, 2026, Jijini Dodoma, amesema Rais Dk. Samia Suluhu Hassan anayajali makundi hayo kwa maneno na kwa matendo, ndiyo maana ameamua kuongeza asilimia za mikopo yao.

"Uwezeshaji wananchi kiuchumi hasa makundi ya wanawake, vijana na wenye mahitaji maalum ni miongoni mwa vipaumbele vya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, ameona asilimia kumi haitoshi, ameongeza asilimia tano zaidi ili kuhakikisha makundi hayo yananufaika na fursa za kiuchumi kwa ustawi wao," amesema Chatanda.

Sambamba na hilo, Chatanda amesema katika mipango ya maendeleo ni vyema kuhakikisha makundi yote yanajumuishwa ili maendeleo tarajiwa yaweze kugusa watu wote kwani hayo ndiyo maendeleo lenye tija kwa Taifa.

"Tanzania tunajenga uchumi shindani na jumuishi, kwa kuhakikisha hilo linafikiwa, ndiyo maana makundi haya yanapewa kipaumbele kwani mafanikio yao yana mchango katika ujenzi wa uchumi wa Taifa zima," amesema.

Kadhalika, Chatanda amesisitiza makundi hayo wapewe mafunzo ya kutosha ya kiujasiriamali ili waweze kutumia vyema mikopo hiyo katika kujiletea maendeleo.

"Maofisa wetu wa maendeleo ya jamii ngazi za kata na wilaya kwa kushirikiana na taasisi za fedha kama mabenki, watoe mafunzo ya namna bora ya kufanya biashara na shughuli nyingine za kiuchumi, ili waweze kuwa na uwezo wa kurejesha mikopo hiyo," amesisitiza.

Katika mabadiliko chanya yaliyofanyika katika bajeti ya mwaka 2026/2027, ni kuongeza asilimia za mikopo kutoka kumi hadi 15 ili kuwezesha makundi hayo kunufaika zaidi kiuchumi likiwepo suala la uboreshaji wa mazingira ya kufanyia shughuli zao za kiuchumi. 



Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma 

Serikali imechukua Hatua Kudhibiti Migogoro ya Wakulima na Wafugaji Mto Lukuledi Ndanda

Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI imesema inatambua changamoto ya uvamizi wa wafugaji katika maeneo ya wakulima katika ushoroba wa Mto Lukuledi, Jimbo la Ndanda, hususan wakati wa ukame ambapo migogoro ya matumizi ya ardhi huongezeka.

Akijibu swali bungeni leo Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI) Dkt  Jafar Seif ameeleza kuwa Serikali kwa kushirikiana na Mamlaka za Serikali za Mitaa pamoja na vyombo vya ulinzi na usalama imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kudhibiti hali hiyo ili kuhakikisha amani na utulivu vinadumishwa kati ya wakulima na wafugaji.

Serikali imeeleza kuwa moja ya hatua kubwa zilizochukuliwa ni pamoja na kupima na kutenga maeneo maalum ya malisho yenye ukubwa wa takribani hekta 129,489.48 katika vijiji 30 vya Mkoa wa Lindi, ikiwemo vijiji vilivyo karibu na bonde la Mto Lukuledi, Ndanda. Hatua hii inalenga kupunguza msongamano wa mifugo katika maeneo ya kilimo na kuzuia migogoro inayojitokeza mara kwa mara.

Aidha, Serikali inaendelea kutoa elimu kwa wafugaji kuhusu umuhimu wa kuachana na ufugaji wa kuhamahama na badala yake kuelekea katika ufugaji wa kisasa unaozingatia tija na biashara. Elimu hiyo inalenga pia kubadilisha mtazamo kuhusu matumizi bora ya ardhi na uhifadhi wa mazingira.

Serikali imetoa wito kwa wafugaji kote nchini kuhakikisha wanazingatia mipango ya matumizi bora ya ardhi pamoja na kutumia kikamilifu maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya malisho kwa kuyaendeleza kupitia kuondoa vichaka na kupanda malisho yanayoendana na ikolojia ya maeneo husika.

Kwa mujibu wa Serikali, utekelezaji wa mikakati hiyo utasaidia kuhakikisha upatikanaji wa malisho ya kutosha mwaka mzima, kupunguza migogoro ya mara kwa mara kati ya wakulima na wafugaji, na hatimaye kuimarisha amani na maendeleo endelevu katika maeneo ya vijijini.



NA DENIS MLOWE IRINGA


ZAIDI ya vijana 200 kutoka vijiji 61 vinavyozunguka Shamba la Miti la Taifa la Sao Hill wilayani Mufindi, mkoani Iringa, wamehitimu mafunzo maalumu ya kukabiliana na majanga ya moto wa misitu ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha ulinzi wa rasilimali za misitu na mazingira kwa ujumla.

Mafunzo hayo yametolewa baada ya kufanyika mchakato wa usaili uliowahusisha zaidi ya vijana 400 waliojitokeza kupima utimamu wa mwili na akili kwa lengo la kushiriki katika kikosi cha kukabiliana na moto wa misitu hatua hiyo imeelezwa kuwa ni mkakati wa kuhakikisha kunakuwa na nguvu kazi ya kutosha yenye uelewa wa masuala ya usalama wa misitu katika maeneo yanayozunguka shamba hilo kubwa la miti.

Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Msaidizi wa Mhifadhi Mkuu wa Shamba la Miti la Taifa la Sao Hill, PCO Said Singano, alisema ushirikishwaji wa vijana kutoka vijiji vinavyozunguka shamba hilo ni njia bora ya kujenga uelewa wa pamoja kuhusu umuhimu wa kulinda misitu na kuzuia hasara zinazoweza kusababishwa na moto.

Alisema moto wa misitu umekuwa tishio kubwa katika maeneo mbalimbali ya misitu nchini, hivyo ni muhimu kuendelea kutoa elimu na mafunzo kwa wananchi wanaoishi karibu na maeneo hayo ili wawe sehemu ya suluhisho la changamoto hiyo.
Aliongeza kuwa vijana waliopatiwa mafunzo wamefundishwa mbinu mbalimbali za kutambua vihatarishi vya moto, namna ya kuzuia kuenea kwa moto pamoja na hatua za haraka za kuchukua pindi moto unapozuka.

Singano alisema kuwa ushiriki wa wananchi katika shughuli za uhifadhi umeendelea kuleta matokeo chanya kwa kuwa jamii imekuwa na uelewa mkubwa zaidi kuhusu thamani ya misitu katika maendeleo ya kiuchumi na uhifadhi wa mazingira.

Alibainisha kuwa Shamba la Miti la Taifa la Sao Hill linaendelea kushirikiana na vijiji vinavyolizunguka ili kuhakikisha misitu inalindwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Kwa upande wake, Afisa wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Wilaya ya Mufindi, Sajenti Guntramu Mlenge, alisema ushirikiano uliopo kati ya Jeshi la Zimamoto na Uokoaji pamoja na Shamba la Miti la Sao Hill umechangia kwa kiasi kikubwa kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu namna ya kujikinga na majanga ya moto.

Alisema kupitia mafunzo hayo, vijana wamepata maarifa ya kutumia vifaa vya kuzimia moto, kutengeneza njia za kuzuia moto kuenea pamoja na mbinu za kufanya doria katika maeneo yenye hatari kubwa ya kutokea kwa moto. A

Aidha, alieleza kuwa elimu hiyo itawasaidia vijana kuwa mabalozi wa usalama wa mazingira katika vijiji vyao.

Baadhi ya vijana walioshiriki mafunzo hayo wameeleza kufurahishwa na fursa waliyoipata wakisema kuwa imewaongezea ujuzi na kuwapa nafasi ya kushiriki moja kwa moja katika shughuli za kulinda misitu.

Walisema maarifa waliyojifunza yatawasaidia kutoa elimu kwa wananchi wengine kuhusu madhara ya moto wa misitu na umuhimu wa kuhifadhi mazingira.

Hatua ya kuwajengea uwezo vijana katika maeneo yanayozunguka Shamba la Miti la Taifa la Sao Hill inaonekana kuwa sehemu muhimu ya mkakati wa kupunguza matukio ya moto wa misitu ambayo yamekuwa yakisababisha hasara kubwa kwa mazingira, uchumi na maendeleo ya jamii.

Serikali na wadau wa uhifadhi wanaamini kuwa ushiriki wa wananchi, hususan vijana, ni nguzo muhimu katika kuhakikisha misitu inalindwa na kuendelea kuwa rasilimali yenye manufaa kwa taifa.









Top News