Na Belinda Joseph- Dodoma.

Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) umeendelea kuwa nguzo muhimu katika kusogeza huduma za mawasiliano karibu na wananchi, hususan waishio maeneo ya vijijini yasiyo na mvuto wa kibiashara kwa kampuni za mawasiliano.

Akizungumza wakati wa maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, Mhandisi Wilfred Charles kutoka UCSAF Juni 21, 2026, amesema ushiriki wao katika maadhimisho hayo unalenga kuielimisha jamii kuhusu majukumu na miradi mbalimbali inayotekelezwa na mfuko huo katika kuboresha huduma za mawasiliano nchini.

Amesema UCSAF kwa kushirikiana na Serikali imekuwa ikitoa ruzuku kwa watoa huduma za mawasiliano ili kuhakikisha huduma hizo zinafika katika maeneo ya vijijini ambayo kwa kawaida hayavutii uwekezaji wa kibiashara.

Ameeleza kuwa Mbali na ujenzi wa miundombinu ya mawasiliano, UCSAF pia inatekeleza mradi wa utoaji wa huduma za WiFi katika maeneo ya wazi, pamoja na kupanua usikivu wa Redio ya Taifa na redio za kijamii katika maeneo mbalimbali nchini, hatua hiyo inalenga kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi na huduma za habari kwa urahisi zaidi.

Katika sekta ya elimu, UCSAF imefanikiwa kufikisha vifaa vya TEHAMA katika shule zaidi ya 1,000 za msingi, sekondari na vyuo nchini, ambazo zimeunganishwa na huduma ya intaneti huku wanafunzi wakipatiwa kompyuta ili kuwajengea uwezo wa kutumia teknolojia za kidigitali na kuongeza ushindani wao katika uchumi wa kidigiti.

Aidha, amesema mfuko huo unaendelea kutoa mafunzo ya TEHAMA kwa walimu ili kuwawezesha kufundisha kwa ufanisi zaidi masomo yanayohusiana na teknolojia pamoja na kutumia mifumo ya kidigitali katika utekelezaji wa majukumu yao.

Mhandisi Charles amesema juhudi hizo zinaendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, hususan lengo la nne ambalo linaweka mkazo katika matumizi ya TEHAMA na kuongeza upatikanaji wa huduma za serikali kwa wananchi wa maeneo ya vijijini.

Kwa upande wa mafanikio ya mawasiliano, amebainisha kuwa tangu kuanzishwa kwa UCSAF, zaidi ya minara 2,000 ya mawasiliano imejengwa katika maeneo ya vijijini, pia mradi wa ujenzi wa minara 758 uliokamilika na kuzinduliwa na Rais Samia Suluhu Hassan umewezesha zaidi ya wananchi milioni 8.5 kupata huduma za mawasiliano.

Sambamba na hilo, UCSAF imeboresha teknolojia ya mawasiliano kwa kupandisha hadhi ya minara 304 iliyokuwa ikitoa huduma za 2G pekee na kuiwezesha kutoa huduma za 3G na 4G, hatua iliyoongeza kasi na ubora wa mawasiliano kwa wananchi wengi zaidi.

Mhandisi Charles amewakaribisha wananchi kutembelea banda la UCSAF katika maadhimisho hayo ili kupata elimu kuhusu huduma zinazotolewa na mfuko huo, pamoja na kutoa taarifa za maeneo ambayo bado hayajafikiwa na huduma za mawasiliano.

"Malengo yetu ni kuhakikisha kila Mtanzania, awe wa mjini au kijijini, anapata huduma bora za mawasiliano kwa usawa".


Zaidi ya wananchi 300 wametembelea banda la Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) tangu kuanza kwa Wiki ya Utumishi wa Umma, wakipata elimu na ufafanuzi kuhusu utekelezaji wa miradi mbalimbali ya barabara katika maeneo yao, hatua hiyo imeendelea kuimarisha uhusiano kati ya wananchi na taasisi hiyo huku ikitoa fursa ya kusikiliza na kutatua changamoto zinazowakabili wananchi moja kwa moja.

Akizungumza katika maonesho hayo, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano kwa Umma wa TARURA, Catherine Sungura, amesema wananchi wanaowasilisha kero zao huunganishwa moja kwa moja na mameneja wa maeneo husika ili kupata maelezo ya kina pamoja na ufumbuzi wa haraka, ameeleza lengo ni kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi kuhusu miradi inayotekelezwa na maendeleo yake.

Katika mwendelezo wa Wiki ya Utumishi wa Umma unaoendelea Jijini Dodoma hadi Juni 23, Sungura alieleza kuwa mwananchi kutoka eneo la Kimara amewasilisha maswali kuhusu maendeleo ya miundombinu ya barabara katika eneo lao , amesema TARURA imekuwa ikitoa ufafanuzi wa kina kwa kila mwananchi anayefika kwenye banda hilo.

Akizungumzia barabara ya King'ong'o iliyopo Kimara, Wilaya ya Ubungo jijini Dar es Salaam, Sungura amesema ujenzi wa barabara ya zege unaoanzia eneo la TRA kuelekea King'ong'o unaendelea vizuri, amebainisha kuwa amewasiliana na Meneja wa TARURA Wilaya ya Ubungo na amewahakikishia wananchi kuwa kilomita 1.6 pekee ndizo zimebaki kukamilishwa, huku mita 800 zikitarajiwa kujengwa mwanzoni mwa mwaka mpya wa fedha kuanzia Julai na sehemu iliyobaki kukamilishwa katika awamu inayofuata.

Amesisitiza kuwa TARURA itaendelea kuhakikisha miundombinu ya barabara inaboreshwa ili kurahisisha mawasiliano na usafiri kwa wananchi, huku akieleza kuwa barabara bora zinachochea upatikanaji wa huduma za kijamii, biashara na shughuli nyingine za maendeleo jambo ambalo ni muhimu katika kuinua ustawi wa jamii na kukuza uchumi wa maeneo mbalimbali nchini.


Wananchi nchini wametakiwa kuwa waangalifu na taarifa pamoja na ushauri wanaoupata kupitia mitandao ya kijamii, kwani si kila elimu inayotolewa mtandaoni ni sahihi au inatolewa na wataalamu wenye sifa stahiki.

Wito huo umetolewa na Mkuu wa Chuo cha Ustawi wa Jamii, Dkt. Joyce Nyoni, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma Juni 21, 2026, katika mwendelezo wa maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma.

Dkt. Nyoni amesema kumekuwa na ongezeko la watu wanaotoa ushauri na elimu mbalimbali mtandaoni bila kuwa na taaluma husika, jambo ambalo linaweza kuwasababisha wananchi kupata huduma zisizo sahihi na hatimaye kufanya hali zao kuwa mbaya zaidi.

Amesisitiza kuwa wananchi wanapaswa kutafuta huduma na ushauri kutoka kwa wataalamu waliopo katika mifumo rasmi ya serikali na taasisi zinazotambulika ili kuhakikisha wanapata msaada unaozingatia misingi ya kitaalamu.

Akizungumzia nafasi ya chuo hicho, Dkt. Nyoni amesema Chuo cha Ustawi wa Jamii kinaendelea kutoa mafunzo katika taaluma za ustawi wa jamii na saikolojia, huku kikizalisha wataalamu mahiri wanaoweza kusaidia jamii kukabiliana na changamoto mbalimbali za kijamii na kisaikolojia.

Ameeleza kuwa wanafunzi wa chuo hicho hujengewa uwezo wa kitaaluma na vitendo kupitia ushiriki wao katika matukio mbalimbali ya kijamii pamoja na majanga, hatua inayowasaidia kuwa wataalamu wenye uzoefu wa kutosha katika kutoa huduma kwa jamii.

Aidha, amesema katika kila ngazi ya utawala kuanzia kata hadi taifa kuna maafisa ustawi wa jamii ambao wananchi wanaweza kuwafikia kwa ajili ya kupata ushauri na huduma stahiki zinazoweza kuwasaidia kujenga maisha bora na kutatua changamoto wanazokabiliana nazo.

Dkt. Nyoni pia amesema Chuo cha Ustawi wa Jamii, kilicho chini ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, kinaendelea na zoezi la udahili kwa wanafunzi wanaotaka kujiunga na masomo mbalimbali yanayotolewa chuoni hapo.

Ametoa rai kwa vijana na wananchi wenye sifa kutumia fursa hiyo kujiunga na chuo hicho ili kupata elimu na ujuzi utakaowawezesha kuwa sehemu ya wataalamu wanaochangia ustawi wa jamii na maendeleo ya taifa.







Na Seif Mangwangi, Michuzi TV Arusha

WANAFUNZI wanaofanya ubunifu wa matumizi ya teknolojia mbalimbali katika chuo cha ufundi Arusha (ATC), wametakiwa kusoma Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kuielewa na kuona fursa zilizopo ndani yake na kufanya bunifu zao kutokana na malengo ya dira hiyo.

Hayo yameelezwa Juni 19, 2026 na Mkuu wa chuo cha ufundi Arusha Profesa Musa Chacha katika hotuba yake ya kufungua wiki ya maonyesho ya ubunifu yanayoandaliwa kila mwaka chuoni hapo.

Profesa Chacha amesema dira ya Taifa 2050 imeainisha maeneo ambayo yanapaswa kuendelezwa kwaajili ya Maendeleo ya Watanzania hivyo wanafunzi wanaofanya bunifu chuoni hapo wanapaswa kuyasoma na kuyajua na kuyafanyia ubunifu.

Amesema kutokana na kazi nzuri ya ubunifu ambayo imekuwa ikifanywa na wanafunzi chuoni hapo, chuo kimepanga kujenga jengo maalum la ghorofa nne ambalo litatumika kwaajili ya shughuli za ubunifu.

“ Kwa kushirikiana na Serikali ya Italia hivi karibuni tunatarajia kujenga jengo kubwa la ghorofa nne ambalo litatumika kwaajili ya shughuli za ubunifu( innovation), hapa chuoni hatutaki hivi vipaji vyenu vipotee,” amesema.

Aidha Profesa Chacha amesema chuo kinaendelea na ujenzi wa karakana ( industrial workshop), ambayo itatumika kutengeneza mitambo bunifu itakayokuwa ikigunduliwa na wanafunzi chuoni hapo kwaajili ya kuuzwa na kwamba tayari mashine zitakazotumika katika karakana hiyo zipo njiani kufika chuoni hapo.

“ Hivi sasa tumeamua kuendeleza bunifu zote zitakazobuniwa na wanafunzi Kwa kuzizalisha na kuziingiza sokoni, tutakuwa na kiwanda hapa hapa chuoni na wote mnaofanya ugunduzi huu tutaendelea kuwafuatilia na kuona namna mnafaidika na bunifu zenu, tutawashika mkono popote mtakapoenda,” amesema Profesa Chacha.

Aidha amesema chuo kinakamilisha jengo la hospitali itakayokuwa ikitibia wanafunzi chuoni hapo lakini pia chuo kipi kwenye mikakati ya kujenga jengo litakalojulikana kama innovation center ambalo litakuwa maalum kwaajili ya ugunduzi na uzalishaji wa vifaa tiba vya hospitalini ( biomedical engineering).

Awali akimkaribisha mgeni rasmi Makamu mkuu wa chuo, Dkt Yusuph Mhando alisema katika maonyesho ya mwaka huu ambayo ni awamu ya tatu tangu kuanzishwa, jumla ya bunifu 75 ziliingia kwenye ushindani.

Amesema kati ya bunifu hizo, bunifu 20 zilihusiana na teknolojia ya habari na mawasiliano(Tehama), umeme 15, mitambo na magari 19, sayansi timizi 8, ujenzi na barabara13 na kwamba baada ya majaji kupitia bunifu hizo jumla ya bunifu 19 pekee ziliweza kuingia fainali.

Amesema mshindi wa kwanza ametoka katika fani ya mitambo aliyegundua mashine inayojulikana kama ( Energy trauma kit), akifuatiwa na Tehama ambaye amegundua mashine ya kupima uoni wa macho ( VR acute test),

Aidha amesema maonyesho hayo ni muhimu Kwa Taifa Kwa kuwa yamekuwa yakikuza ujuzi wa wanafunzi chuoni hapo Kwa kuweza kuonyesha Kwa vitendo kile ambacho wamekuwa wakifundishwa darasani.

“ Katika bunifu hizi, Kuna vijana wametengeneza mfumo wa kupiga kura wakati wa uchaguzi ukiwa nyumbani, teknolojia hii ikiweza kuboresha itaweza kusaidia sana katika eneo hili,” amesema.

Amesema ni tegemeo la chuo kuwa bunifu hizo zitafikia jamii na kutatua kero mbalimbali inazizikabili na hivyo chuo kitaendelea kuimarisha na kuendeleza vipaji vya wanafunzi hao.



 

Tume ya Ushindani (FCC) imesema imeanza mpango wa kuanzisha klabu za elimu ya ushindani, ulinzi wa mlaji na udhibiti wa bidhaa bandia katika shule za msingi, sekondari na taasisi za elimu ya juu ili kujenga kizazi chenye uelewa wa masuala hayo.

Akizungumza na waandishi wa habari Juni 20, 2026, katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea jijini Dodoma, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma wa FCC, Bi. Roberta Feruzi, amesema mpango huo utatekelezwa kupitia klabu zitakazojulikana kama Ushindani School Club. 

Amesema lengo la mpango huo ni kuwafikia wanafunzi mapema na kuwajengea uelewa kuhusu ushindani, haki za mlaji na namna ya kufanya maamuzi sahihi wanaponunua bidhaa au kupata huduma.

Feruzi amesema elimu hiyo itawasaidia wananchi kutambua bidhaa bandia, kulinda soko dhidi ya udanganyifu na kuwawezesha watumiaji kuchagua bidhaa salama na zenye ubora.

Ameeleza kuwa uelewa wa masuala ya ushindani na ulinzi wa mlaji utasaidia wananchi kufanya uchaguzi bora wa bidhaa na huduma, huku sekta binafsi ikiendelea kuchangia katika uzalishaji na ukuaji wa uchumi.

Aidha, amesema utoaji wa elimu hiyo utaendelea kupitia ofisi za kanda za FCC zilizopo Mwanza, Arusha, Mbeya, Dodoma na Dar es Salaam kwa lengo la kuhakikisha wananchi katika mikoa yote ya Tanzania Bara wanapata elimu hiyo.




Katika kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050 inayolenga kuhakikisha wananchi wanapata makazi bora na ya gharama nafuu, Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) umeendelea kutekeleza mpango wa ujenzi wa nyumba za gharama nafuu ili kuwawezesha wananchi, hususan vijana, kumudu kumiliki makazi.

Akizungumza katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika kitaifa katika viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma, Mkurugenzi wa Huduma Saidizi wa TBA, Bi. Amina Lumuli, amesema kuwa TBA tayari imeanza kutekeleza miradi ya nyumba za gharama nafuu katika mkoa wa Dar es Salaam.

Bi. Lumuli ametaja Mradi wa Temeke Kota kuwa ni miongoni mwa miradi hiyo, akibainisha kuwa utekelezaji wa mpango huo utaendelea katika maeneo mbalimbali nchini.

"Tunawakaribisha wawekezaji kuja kushirikiana nasi ili kwa pamoja tuweze kufanikisha lengo la Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 la kuhakikisha wananchi wanapata makazi bora na ya gharama nafuu," amesema Bi. Lumuli.

Aidha, Bi. Lumuli amesema utekelezaji wa mradi huu unatokana na dhamira ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuhakikisha wananchi wanapata makazi bora na yenye gharama nafuu.

Amesema TBA itaendelea kuhakikisha makundi yote, yakiwemo makundi maalum, yanafikiwa na kunufaika na programu hii ya nyumba za gharama nafuu.

Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA) imeeleza kuwa uzalishaji wa pareto nchini bado haujakidhi mahitaji ya viwanda vya ndani, huku Tanzania ikizalisha wastani wa tani 4,000 za maua makavu kwa mwaka dhidi ya mahitaji ya tani 9,000, hali hiyo imeacha upungufu wa tani 5,000, sawa na zaidi ya nusu ya mahitaji yaliyopo.

Akizungumza Juni 20, 2026,  katika maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea jijini Dodoma, Afisa Kilimo Mwandamizi wa COPRA, Sikitu Mwakeja, alisema kuna fursa kubwa kwa wakulima, vijana na wawekezaji wa sekta binafsi kuingia katika kilimo cha pareto kutokana na soko la uhakika lililopo nchini.

Mwakeja alibainisha kuwa bei ya maua makavu ya pareto imeendelea kuwa ya kuvutia, ikifikia kati ya Sh4,000 na Sh5,000 kwa kilogramu kulingana na kiwango cha ubora, ameongeza kuwa kwa kufuata mbinu bora za kilimo, ekari moja inaweza kutoa hadi kilogramu 500 za maua makavu kwa msimu, hivyo kulifanya zao hilo kuwa miongoni mwa mazao yenye tija kwa wakulima.

Kwa sasa, uzalishaji mkubwa wa pareto unafanyika katika mikoa ya Mbeya, Songwe, Njombe, Iringa, Manyara, Arusha na Kilimanjaro, COPRA imewahimiza wadau mbalimbali kutumia fursa ya mahitaji makubwa yaliyopo sokoni ili kuongeza uzalishaji, kupunguza pengo lililopo na kuimarisha mchango wa zao hilo katika ukuaji wa uchumi wa taifa kupitia mnyororo wake wa thamani.



Leo tumefungua rasmi ziara ya Kamati ya Utekelezaji ya Jumuiya ya Wazazi Mkoa wa Dar es Salaam kwa kuanza katika Jimbo la Kibamba.

Akizungumza na viongozi wa Kata na Matawi, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Mkoa wa Dar es Salaam, Khadija Ally, amewashukuru kwa moyo wa kujitolea, uzalendo, mshikamano na ushiriki wao wa hali na mali katika kufanikisha shughuli za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.

“Uzalendo wenu, mshikamano wenu, kujitolea kwenu na imani yenu kwa Chama Cha Mapinduzi vimechangia kwa kiwango kikubwa mafanikio ya chama na ushindi uliopatikana.”

Ziara hii inalenga kuwashukuru viongozi na wanachama wetu, kuimarisha umoja na mshikamano, pamoja na kuhamasisha ari ya utendaji kazi katika kuendelea kuijenga Jumuiya ya Wazazi na Chama Cha Mapinduzi kwa maendeleo ya Taifa letu.
Katika ziara hii, Kamati ya Utekelezaji ya Mkoa wa Dar es Salaam chini ya Mwenyekiti wake Khadija Ally itatembelea Kata zote 102 za Mkoa wa Dar es Salaam na kugawa tuzo za pongezi na shukrani kwa viongozi wa Kata kwa mchango wao mkubwa katika kuimarisha chama.

Tunawathamini, tunawapenda, na tunaamini kuwa nguvu ya Chama Cha Mapinduzi ipo kwa wanachama wake wenye uzalendo, uaminifu, mshikamano na imani thabiti kwa chama chao.

#JumuiyaYaWazaziDSM
#UmojaMshikamanoNaMaendeleo
#CCMKaziIendelee
#ZiaraYaShukrani2026



 









no image

Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) umesema umeendelea kutekeleza jukumu lake la kuwaunganisha wananchi na huduma muhimu za kijamii pamoja na fursa za kiuchumi kupitia ujenzi na uboreshaji wa miundombinu ya barabara na madaraja nchini.

Akizungumza katika maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma Jijini Dodoma, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano kwa Umma wa TARURA, Catherine Sungura, alisema lengo kuu la wakala huo ni kuwafungulia wananchi njia za kufikia huduma mbalimbali za kijamii, masoko na kuchochea ukuaji wa uchumi wa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.

Alisema hadi sasa TARURA imefanikiwa kujenga zaidi ya madaraja ya mawe 490 katika maeneo mbalimbali nchini, hatua iliyochangia kuboresha mawasiliano na usafiri kwa wananchi.

Aidha, Sungura alisema wakala huo umefanikiwa kurejesha kwa zaidi ya asilimia 70 mawasiliano ya barabara katika maeneo yaliyoathiriwa na mvua za El Nino zilizochangia mafuriko na kusababisha uharibifu wa miundombinu.

Aliongeza kuwa mafanikio hayo yamewezekana baada ya Serikali kupata ufadhili kutoka Benki ya Dunia, ambao umewezesha utekelezaji wa miradi ya kurejesha miundombinu na mawasiliano ya barabara kutoka ngazi ya vijiji hadi taifa kwa ujumla.

Na Janeth Raphael MichuziTv.

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dkt. Abdulmajid Nsekela, amesema benki hiyo imejipanga kikamilifu kuhakikisha Watanzania wananufaika na fursa za kiuchumi zitakazotokana na mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027 yatakayofanyika Tanzania, Kenya na Uganda.

Akizungumza katika Bunge Grand Bonanza lililofanyika jijini Dodoma, Dkt. Nsekela amesema CRDB itaendelea kutoa mitaji na huduma mbalimbali za kifedha zitakazowawezesha wananchi, wafanyabiashara na wawekezaji kutumia kikamilifu fursa zitakazotokana na mashindano hayo.

Amesema AFCON si tukio la michezo pekee bali ni jukwaa muhimu la kiuchumi litakalovutia wageni wengi kutoka ndani na nje ya Afrika, hivyo kuongeza mahitaji ya huduma mbalimbali zikiwemo malazi, usafiri, chakula na biashara nyingine ndogondogo na za kati.

"AFCON ina fursa nyingi za kiuchumi. Huu si wakati wa kusherehekea michezo pekee, bali ni fursa ya kukuza biashara, kuongeza ajira na kuinua uchumi wa wananchi. CRDB imejipanga kuhakikisha Watanzania wanapata mitaji na huduma zitakazowawezesha kunufaika na fursa hizo," alisema Dkt. Nsekela.

Aidha, aliipongeza Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa ya kutunga sheria zinazochochea maendeleo ya Taifa na kuimarisha mazingira ya uwekezaji na biashara nchini.

Pia alimpongeza Waziri wa Fedha kwa kuwasilisha bajeti ya Serikali ambayo alisema itaendelea kuboresha maisha ya Watanzania na kuchochea ukuaji wa uchumi, huku akimpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa maono yake ya maendeleo yanayoendelea kufungua fursa mbalimbali za kiuchumi nchini.

Dkt. Nsekela amesema uwepo wa mabalozi wa nchi mbalimbali katika bonanza hilo ni ishara ya mahusiano mazuri ya kidiplomasia na kibiashara ambayo Tanzania imeendelea kujenga na kuyaimarisha kwa miaka mingi.

Amesema michezo ni chombo muhimu cha kuimarisha mshikamano, urafiki na ushirikiano miongoni mwa watu wa mataifa tofauti, huku akisisitiza kuwa ushiriki wa wadau mbalimbali katika bonanza hilo unaonesha namna michezo inavyoweza kuunganisha jamii.

Mkurugenzi huyo amebainisha kuwa CRDB imekuwa mshirika wa maendeleo kwa zaidi ya miongo mitatu na imeendelea kuwa zaidi ya benki kwa kusaidia ukuaji wa biashara, uwekezaji na ajira nchini.

Amengeza kuwa benki hiyo itaendelea kushirikiana na Serikali pamoja na Bunge katika kuhakikisha Tanzania inanufaika kikamilifu na fursa za kiuchumi zinazotokana na matukio makubwa ya kimataifa.

Katika hatua nyingine, Dkt. Nsekela ametoa shukrani kwa uongozi wa Bunge kwa kuendelea kuiamini CRDB na kuipa nafasi ya kuwa mdau mkuu wa Bunge Bonanza, akiahidi kuwa benki hiyo itaendelea kuunga mkono jitihada za maendeleo ya Taifa kupitia sekta za michezo, biashara na uchumi.

Bunge Grand Bonanza lilihusisha ushiriki wa wabunge, watumishi wa Bunge, taasisi mbalimbali za umma na binafsi pamoja na mabalozi wa nchi rafiki, ambapo washiriki walishiriki michezo mbalimbali kwa lengo la kuimarisha afya, mshikamano na ushirikiano.







Na Janeth Raphael MichuziTv 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema Tanzania na Namibia zimejipanga kuimarisha zaidi ushirikiano wa kiuchumi kwa lengo la kuongeza kiwango cha biashara na uwekezaji kati ya mataifa hayo mawili. 

Amesema hatua hiyo inalenga kufungua fursa mpya za maendeleo kwa sekta binafsi na wananchi kwa ujumla.

Akizungumza katika Jukwaa la Biashara na Uwekezaji kati ya Tanzania na Namibia lililofanyika jijini Dar es Salaam, Rais Samia amesema licha ya uhusiano wa muda mrefu wa kidiplomasia kati ya nchi hizo, bado kiwango cha biashara hakijafikia uwezo unaolingana na fursa zilizopo pande zote mbili.

Amesema viongozi wa Tanzania na Namibia wamekubaliana kuharakisha utekelezaji wa makubaliano mbalimbali ya ushirikiano, ikiwemo Hati ya Makubaliano (MoU) inayolenga kuimarisha biashara na kukuza sekta ya biashara ndogo, za kati na ndogo kabisa ili kuimarisha uchumi jumuishi.

Rais Samia amebainisha kuwa Tanzania inaendelea kuwa moja ya nchi zenye uchumi unaokua kwa kasi barani Afrika, na ina nafasi ya kipekee kama lango la biashara kwa nchi za Afrika Mashariki, Kati na Kusini. Amesema hali hiyo inatoa fursa kubwa kwa Namibia na wawekezaji wake kutumia Tanzania kama kituo muhimu cha usafirishaji na uwekezaji.

Katika kuimarisha mazingira ya biashara, Rais Samia amesema Serikali ya Tanzania imeendelea kufanya maboresho mbalimbali ikiwemo kurahisisha usajili wa kampuni, ambapo sasa mchakato huo unakamilika ndani ya saa 24, hatua inayolenga kuvutia wawekezaji zaidi wa ndani na nje ya nchi.

Aidha, amezitaja sekta za usafirishaji na huduma za bandari kuwa miongoni mwa maeneo yenye fursa kubwa za ushirikiano, akibainisha kuwa maboresho yanaendelea katika Bandari ya Dar es Salaam huku mipango ya kuendeleza Bandari ya Bagamoyo na bandari nyingine ikiendelea ili kuongeza ufanisi wa biashara za kikanda.

Katika sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi, Rais Samia amesema Tanzania ina ardhi kubwa na rasilimali nyingi, huku Namibia ikiwa na uzoefu mkubwa katika sekta ya mifugo na uvuvi, jambo linalofungua nafasi ya ushirikiano wenye manufaa kwa pande zote mbili.

Pia amesisitiza umuhimu wa sekta ya mafuta na gesi kama eneo jingine la kimkakati lenye fursa kubwa za uwekezaji, akieleza kuwa mataifa hayo yote mawili yana rasilimali hizo na yanahitaji ushirikiano katika teknolojia, uwekezaji na uendelezaji wa sekta hiyo.

Hata hivyo Rais Samia amesisitiza kuwa Tanzania itaendelea kuboresha mazingira rafiki ya uwekezaji kwa kuhakikisha kunakuwa na utulivu, uwazi na sera imara zitakazowezesha kuvutia mitaji ya muda mrefu kwa manufaa ya wananchi wa Tanzania na Namibia.



Na Janeth Raphael -MichuziTv 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametoa wito kwa wafanyabiashara wa Tanzania na Namibia kuchangamkia fursa zilizopo katika mataifa hayo mawili ili kuongeza kasi ya biashara, uwekezaji na ushirikiano wa kiuchumi.

Rais Samia ametoa kauli hiyo leo Jumamosi, Juni 20, 2026, kufuatia mazungumzo rasmi kati yake na Rais wa Jamhuri ya Namibia, Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah, yaliyolenga kuimarisha zaidi uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi kati ya nchi hizo mbili za Afrika.

Akizungumza baada ya mazungumzo hayo, Rais Samia amesema Tanzania na Namibia zina historia ndefu ya ushirikiano iliyojengwa tangu harakati za ukombozi wa Bara la Afrika, akisisitiza kuwa sasa ni wakati wa historia hiyo kugeuzwa kuwa faida ya moja kwa moja kwa wananchi kupitia uchumi imara.

Amebainisha kuwa mwaka 2024, thamani ya biashara kati ya Tanzania na Namibia ilikuwa takribani shilingi bilioni 20, akisema bado kuna nafasi kubwa ya kuongeza zaidi kiwango hicho kupitia uwekezaji wa sekta mbalimbali.

Katika mazungumzo yao, viongozi hao walijikita pia katika maeneo ya kimkakati ikiwemo usalama wa chakula, uchumi wa buluu, madini, mafuta na gesi, pamoja na kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji kwa pande zote mbili.

“Niwahamasishe wafanyabiashara wa Tanzania kuchangamkia fursa zilizopo Namibia, na pia wana-Namibia wafanye vivyo hivyo kuja kuwekeza Tanzania,” amesema Rais Samia.

Katika sekta ya uchumi wa buluu, viongozi hao wamesema nchi zote mbili zina rasilimali kubwa za bahari zinazoweza kuchochea ukuaji wa uchumi na kuboresha maisha ya wananchi.

Aidha, wamekubaliana kuimarisha ushirikiano katika sekta ya mafuta na gesi, wakibainisha kuwa sekta hizo zina uwezo mkubwa wa kuleta mageuzi ya kiuchumi katika ukanda wa Afrika.

Pia, mazungumzo yao yaligusia uwezekano wa kuanzishwa kwa safari za ndege za moja kwa moja kati ya Tanzania na Namibia, hatua inayotarajiwa kurahisisha biashara, uwekezaji na kuongeza mtiririko wa utalii kati ya mataifa hayo mawili.

Rais Samia amesisitiza kuwa ushirikiano wa kiuchumi kati ya nchi za Afrika bado ni nguzo muhimu ya maendeleo, akieleza kuwa bara la Afrika lina rasilimali nyingi na nguvu kazi kubwa ya vijana ambayo inaweza kuleta mabadiliko makubwa iwapo itatumika kikamilifu.



Na Karama Kenyunko, Michuzi TV
MKURUGENZI Muendeshaji wa shirika lisilo la kiserikali (MSI) Tanzania, Dkt. Stephen Mutegeki, amesema utekelezaji wa Programu ya Scaling Up Family Planning (SuFP) kwa kipindi cha miaka tisa umechangia kwa kiasi kikubwa kusogeza huduma za afya ya uzazi na uzazi wa mpango karibu na wananchi, hususan wanawake, vijana, watu wenye ulemavu na makundi mengine yaliyokuwa magumu kufikiwa.

Dkt. Mutegeki ameyasema hayo leo jijini Dodoma wakati wa Kongamano la Kujifunza la Programu ya SuFP lililofanyika chini ya kaulimbiu isemayo, “Kudumisha Mafanikio Yaliyopatikana katika Afya ya Uzazi na Uzazi wa Mpango.”

Amesema MSI Tanzania, kama mmoja wa washirika wa utekelezaji wa programu hiyo iliyofadhiliwa na Serikali ya Uingereza kupitia Foreign, Commonwealth and Development Office (FCDO), imejikita katika kuimarisha mifumo ya afya ya umma, kuboresha ubora wa huduma na kujenga uwezo wa wataalamu wa afya ili kuhakikisha huduma bora zinawafikia wananchi wengi zaidi.

Kwa mujibu wa Dkt. Mutegeki, kupitia programu hiyo MSI Tanzania ilipeleka timu 12 za huduma za mkoba katika mikoa 12 ili kufikisha huduma za afya ya uzazi katika maeneo ya pembezoni na magumu kufikika.

Aidha, wauguzi 28 walipangwa katika mikoa 14 kwa ajili ya kutoa ushauri wa kitaalamu na kujenga uwezo wa watumishi wa afya katika vituo vya umma.

Alisema vituo vya afya vya umma 176 vilipatiwa mafunzo na usimamizi wa kitaalamu, huku watoa huduma za afya 469 wakipatiwa mafunzo maalumu ya utoaji wa huduma bora za uzazi wa mpango na afya ya uzazi.

“Zaidi ya wataalamu wa afya 1,180 wamenufaika na programu za uangalizi na ushauri kazini zilizolenga kuimarisha ubora wa huduma,” amesema.

Akizungumzia huduma kwa vijana, Dkt. Mutegeki amesema MSI Tanzania imetekeleza zaidi ya matukio 32 katika taasisi za elimu ya juu pamoja na miradi 32 ya Human-Centred Design iliyolenga kuongeza upatikanaji wa taarifa na huduma za afya ya uzazi kwa vijana na balehe.
Kwa upande wake, Mtaalamu wa Afya ya Mama na Uzazi ambaye pia ni Mkurugenzi Mkazi wa EngenderHealth, Dkt. Moke Magoma, amesema programu hiyo ililenga kuongeza upatikanaji wa huduma jumuishi za uzazi wa mpango kwa makundi mbalimbali ya wananchi.

Amesema huduma hizo pia zilihusisha uchunguzi wa Virusi vya Ukimwi (VVU), utoaji wa msaada kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia pamoja na kuwaelekeza kupata huduma stahiki. Aidha, programu hiyo ilisaidia kuboresha vituo vya afya vya serikali ili kuhakikisha vinatoa huduma bora kwa wanawake waliopoteza ujauzito.

“Tulilenga kufikisha huduma za uzazi wa mpango kwa makundi ambayo hayakuwa yakifikiwa kwa urahisi, hususan vijana balehe, watu wenye ulemavu na wananchi wanaoishi katika maeneo ya mbali,” amesema.

Dkt. Magoma amesema pia walihakikisha mifumo ya utoaji wa huduma inaboreshwa, ukusanyaji wa takwimu unafanyika kwa ufasaha na ubora wa huduma unafuatiliwa kwa karibu kwa kuhamia kutoka mfumo wa makaratasi kwenda mfumo wa kidijitali.
Naye Mwakilishi wa UNFPA Tanzania, Mark Bryan Schreiner, amesema zaidi ya watu milioni 5.2 wamefikiwa na huduma za uzazi wa mpango kati ya mwaka 2017 na 2026.

Amesema hatua hiyo imechangia kuzuia mimba zisizotarajiwa milioni 8.3, utoaji mimba usio salama milioni 2.3 na vifo vya wajawazito 6,511.

Kwa mujibu wa takwimu zilizowasilishwa katika kongamano hilo, programu ya SuFP ilitekelezwa katika mikoa 22 ya Tanzania na kusaidia kuimarisha mifumo ya ugavi wa dawa na vifaa tiba, usimamizi wa taarifa za kidijitali na uwezo wa wahudumu wa afya katika kutoa huduma bora za afya ya uzazi.

Mbali na kuimarisha huduma za afya, programu hiyo ilitoa kipaumbele kwa vijana, watu wenye ulemavu na jamii zilizo katika mazingira magumu kupitia ubunifu mbalimbali, ikiwemo mfumo wa kidijitali wa i-Plan uliorahisisha upatikanaji wa taarifa na huduma za afya ya uzazi.

“Kuna umuhimu wa kuongeza uwekezaji wa ndani katika sekta ya afya ili kuhakikisha mafanikio haya yanaendelea kudumu wakati ambapo misaada ya maendeleo kutoka nje inaendelea kupungua duniani,” amesema.

Programu ya SuFP ilitekelezwa kwa ushirikiano wa UNFPA, MSI Tanzania, EngenderHealth, Pathfinder International, CCBRT, DKT na International Rescue Committee (IRC), kwa ufadhili wa Serikali ya Uingereza kupitia FCDO.

Vichwa vingine vya habari unavyoweza kutumia ni:
SuFP Yafikia Zaidi ya Watu Milioni 5.2 kwa Huduma za Uzazi wa Mpango.



Picha ya pamoja.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, amesema Tanzania ni miongoni mwa nchi chache barani Afrika zilizofanikiwa kusambaza huduma ya umeme  vijijini, hatua ambayo imewezesha wananchi wengi kupata huduma hiyo kutoka ngazi za mikoa, wilaya, kata na vijiji, huku sasa juhudi zikielekezwa katika kufikisha umeme kwenye vitongoji.

Akizungumza na wananchi wa Kata ya Hogoro wilayani Kongwa mkoani Dodoma wakati wa ziara ya kusikiliza na kutatua kero za wananchi, Senyamule alisema serikali inatarajia kupeleka umeme katika vitongoji sita vya kata hiyo katika mwaka ujao wa fedha.

Alieleza kuwa matarajio ya serikali ni kuhakikisha vitongoji vyote vinapata huduma ya umeme ifikapo mwaka 2030, jambo litakalosaidia kuongeza maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi.

“Zamani wananchi walitegemea chemli na vibatari kwa ajili ya mwanga, lakini sasa serikali imeona umuhimu wa kupeleka umeme karibu na wananchi ili waweze kupata mwanga wa uhakika na kufanya shughuli mbalimbali za kiuchumi zinazowaongezea kipato na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.”

Katika sekta ya elimu, Mkuu huyo wa Mkoa alisema Serikali ya Awamu ya Sita imefanikisha ujenzi wa shule nyingi zaidi kuliko vipindi vilivyotangulia, huku akiwataka wazazi na walezi kuhakikisha watoto wote wanapata fursa ya elimu.

Alisisitiza kuwa dhamira ya serikali ni kuona kila Mtanzania anajua kusoma na kuandika katika miaka ijayo ili kuwaandaa wananchi kukabiliana na ushindani wa dunia ya sasa inayokua kwa kasi katika nyanja za sayansi na teknolojia.

“Dunia ya leo imekuwa kama kijiji kutokana na maendeleo ya teknolojia. Elimu na ujuzi ni nyenzo muhimu zinazoweza kumpa mtu fursa ya kufanya kazi na kuishi popote duniani”.

Aidha, Senyamule alisema serikali imeendelea kuboresha huduma za afya kwa kujenga na kuimarisha zahanati, vituo vya afya na hospitali pamoja na kuweka mazingira rafiki ya utoaji huduma.

Kutokana na maboresho hayo, alisema hakuna sababu ya wanawake wajawazito kujifungulia nyumbani kwani huduma bora za afya sasa zinapatikana karibu na wananchi, hatua inayolenga kupunguza vifo vya mama na mtoto wakati wa kujifungua.





Top News