

MichuziBlogV2
Most read Swahili blog on earth
Bonyeza play kuangalia Michuzi TV LiVE
BONYEZA PLAY KUANGALIA AZAM TV LIVE
BONYEZA KUANGALIA CHANNEL TEN LIVE


Na Mwandishi Wetu
MKURUGENZI Mkuu wa Bodi ya Utalii Tanzania(TTB) Ephraim Mafuru amesema kuzinduliwa kwa meli mpya kubwa na ya kisasa ya MV New Mwanza kunakwenda kufungua fursa katika sekta ya utalii ambapo sasa watalii watazunguka nchi za Afrika Mashariki kwa kutumia usafiri wa meli hiyo ambayo ni rahisi na nafuu.
Mafuru ametoa kauli hiyo leo alipokuwa akizungumza baada ya Tanzania kuandika historia kubwa katika uwekezaji ya miundombinu ya usafiri, usafirishaji na utalii katika Bara la Afrika.
“Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imewekeza Sh.bilioni 120 katika meli hii. Watanzania wenzangu na Waafrika kwa ujumla Bodi ya Utalii Tanzania tunatoa mwito tutumie meli hii kuendeleza biashara zetu zinazozunguka katika Afrika Mashariki kwasababu Ziwa Victoria ndio ziwa kubwa kuliko maziwa yote katika Afrika
“Inauwezo wa kubeba mizigo mingi na kusafirisha abiria lakini pia kuleta watalii. Kwawale mlioko sekta ya utalii mtakubaliana nami ya kwamba watalii wanaozunguka katika Afrika Mashariki kutoka Kenya tunawageni 240,000 , na kutoka Uganda ni wageni kama 60,000 na wengi wanatumia barabara ,wengi wanatumia safari za anga
“Leo hii Serikali ya Awamu ya Sita imeidhihirishia dunia ya kwamba watalii sasa wanaweza kuzunguka Afrika Mashariki kwa kutumia usafiri rahisi na nafuu kupitia meli hii ya Mv New Mwanza,”amesema Mafuru kuhusu kuzinduliwa kwa meli hiyo sambamba na fursa ambazo zitapatikana katika kukuza utalii.
Awali wakati anazungumza meli hiyo Mafuru amesema ndani ya wiki mbili zilizopita yameshuhudiwa makubwa katika historia ya nchi yetu na leo katika Jiji la Mwanza Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Mwigulu Nchemba ameongoza viongozi mbalimbali wa Serikali na Chama na wawekezaji walioko ndani ya Tanzania kushuhudia uzinduzi wa meli hiyo kubwa ya MV New Mwanza
“Kwamara ya kwanza katika bara la Afrika yaani vyombo vinavyotumika katika maji baridi katika maziwa Tanzania inakuwa nchi ya kwanza kwa ujenzi na uzinduzi wa meli kubwa MV New Mwanza ambayo leo imezinduliwa jijini Mwanza ikiwa na uwezo wa kubeba abiria 1200 kwa wakati mmoja,magari madogo 20 na magari makubwa matatu
“Sasa unaweza kujiuliza tani 400 za mizigo zina uwezo wa kubebwa na meli hii, kwa Watanzania wenzangu ambao tunaweza kupiga picha tani 400 maana yake nini ? Ukichukua yale magari makubwa semitraila tani 400 ni magari 13.
Hebu piga hesabu msururu wa yale magari ,urefu wa hii meli ni karibu uwanja mmoja wa mpira kwani uwanja wa mmoja wa mpira una mita 92.”
Na WANDISHI WETU
MWENYEKITI wa Jumuiya ya Wazazi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Temeke, Hamis Slim, amewakata viongozi wa mabaraza, kamati za utekelezaji za kata na matawi za jumuiya hiyo kuvunja makundi yaliyotokana na uchaguzi mkuu wa Oktoba 29 , 2029 na kufanyakazi kwa ushirikiano.
Ameyasema hayo Dar es Salaam, leo katika ziara ya Kamati ya Utekelezaji ya Jumuiya hiyo Wilaya ya Temeke katika Kata za Kiburugwa na Kibondemaji inayo lenga kuwashukuru wanachama wa jumuiya hiyo kwa ushindi mkubwa wa CCM na kuimarisha uhai wa jumuiya.
Slim, amesema uchaguzi umekwisha hivyo ni wakati muafaka wa kuvunja makundi, kusameheana, kupendana na kuhudumia jumuiya kwa ufanisi na weledi.
“Tunawapongeza Jumuiya ya Wazazi mmeafanya kazi nzuri katika uchaguzi mkuu na kuipatia ushindi wa kishindo CCM na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan. Sasa ni wakati wa kuleta maendeleo. Tuzike tofauti zetu zilizotokana na uchaguzi. Mwiba ulipoingia ndipo unapotokea,”amesema Slimu.
Pia amewataka kuishi kwa hofu ya Mungu, kuheshimu katiba ya CCM, kanuni na viongozi na wanachama.
“Binadamu anahamika kwa mambo matatu, Jambo la kwanza ni jinsi anavyo jifahamu mwenyewe. Jambo la pili ni namna watu wengine wanavyo mfahamu na jambo la tatu ni nama anavyo fahamika na Mungu. Tusidharauliane kwa sababu mamlaka hata za dunia na viongozi wake zimetoka kwa Mungu,”amesema Slim.
Aidha Slim, ametumia ziara hiyo kutoa pole kwa wanachama wa jumuiya hiyo, CCM na wananchi wote kwa ujumla kwa matukio yaliyojitokeza Oktoba 29, 2025 katika uchaguzi mkuu na kuwakumbusha umuhimu wa kutunza amani ya taifa.
Naye Katibu wa Jumuiya ya Wazazi Wilaya ya Temeke, Emmanuel Itatiro, amewataka viongozi wa jumuiya hiyo katika ngazi za mashina, matawi na kata, kutekeleza wajibu wao kwa kufuata Katiba ya CCM na jumuiya hiyo, kanuni na miongozo.
Pia, amewahimiza kuwajibika ipasanyo hususan kuitisha vikao vya kikatiba na kushughulikia changamoto za wananchi, hususa katika sekta za elimu, afya, malezi na mazingira.
Ziara hiyo ya Kamati ya Utekelezaji ya Jumuiya ya Wazazi Wilaya ya Temeke, itapita katika kata zote za wilaya hiyo.
WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amemwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika ibada ya kumuaga aliyekuwa Gavana wa kwanza wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Mzee Edwin Mtei, akimtaja kuwa kiongozi mahiri, mzalendo na nguzo muhimu katika historia ya uchumi na demokrasia ya Tanzania.
Akizungumza katika ibada hiyo ya mazishi iliyofanyika nyumbani kwa marehemu Tengeru, Dkt. Nchemba alisema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anatambua mchango mkubwa wa marehemu kwa Taifa na Serikali mara zote itaenzi mchango wake mkubwa katika uchumi na demokrasia nchini.
Waziri Mkuu alisema Mzee Mtei alikuwa miongoni mwa Watanzania wachache waliobahatika kuhudumu katika nyadhifa zote kuu za sekta ya fedha, ikiwemo kuwa Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Waziri wa Fedha na mwakilishi wa Tanzania katika taasisi za fedha za kimataifa, mchango uliompa heshima ya kipekee kitaifa na kimataifa.
Alisema katika maisha yake ya utumishi wa umma, marehemu alitambulika kwa kusimamia misingi ya uadilifu, uaminifu, uzalendo, bidii na kumcha Mungu na kwamba mchango wake uliweka msingi imara wa taasisi za kifedha na nidhamu ya uchumi wa Taifa.
Dkt. Nchemba alibainisha kuwa Mzee Mtei pia alikuwa miongoni mwa waasisi wa demokrasia ya vyama vingi nchini, akiwa mwanzilishi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), hatua iliyochangia kwa kiasi kikubwa kuimarisha mfumo wa kisiasa na uhuru wa mawazo nchini.
Katika kuenzi mchango wa marehemu kwa vitendo, Waziri Mkuu alitoa maelekezo mahsusi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo, akisisitiza kuwa hatua hizo ni sehemu ya kudumisha misingi ya maendeleo, haki na uzalendo aliyoyaishi marehemu.
Kuhusu miundombinu ya barabara, Waziri Mkuu alielekeza ukamilishwaji wa taratibu za manunuzi na kuanza mara moja kwa ujenzi wa barabara ya njia nne katika kipande cha Tengeru hadi Usa River, akieleza kuwa mkandarasi anatakiwa kuingia eneo la kazi bila kuchelewa.
Aidha, kwa kipande cha Usa River hadi Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) chenye urefu wa kilomita 28, Waziri Mkuu alisema usanifu wa mradi ulikuwa umefikia takribani asilimia 80, na akaelekeza Wizara ya Ujenzi kwa kushirikiana na TANROADS kukamilisha haraka usanifu uliobaki na kutangaza zabuni mara moja, akisisitiza kuwa fedha za utekelezaji wa mradi huo tayari zipo.
Katika hatua nyingine, aliagiza ukamilishwaji wa barabara na madaraja katika maeneo korofi kati ya Kilimanjaro na Arusha ifikapo Februari 20, 2026, akielekeza Wizara ya Ujenzi na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha kuhakikisha barabara hiyo inafunguliwa na kuanza kutumika kwa lengo la kuondoa adha kwa wananchi.
Kuhusu mgogoro wa ardhi katika eneo la Mringa Estate, Waziri Mkuu alielekeza marekebisho yafanyike ndani ya mwezi mmoja kwa mujibu wa makubaliano ya awali, ili wananchi waliopaswa kunufaika na eneo hilo wapate haki yao. Aliagiza Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Kamishna wa Ardhi pamoja na maafisa ardhi husika kusimamia kikamilifu utekelezaji wa agizo hilo, hususan katika eneo lililonunuliwa na kampuni ya Bajuta Enterprises.
Waziri Mkuu alisisitiza kuwa utekelezaji wa maelekezo hayo ni sehemu ya dhamira ya Serikali ya kuendeleza maendeleo jumuishi, kusimamia haki za wananchi na kudumisha heshima ya viongozi waliolitumikia Taifa kwa uadilifu na uzalendo akiwemo Mzee wetu Mtei.
Na Benny Mwaipaja, Tanga