Na Mwandishi Wetu

KATIKA kuadhimisha siku ya kuzaliwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, siku hii imepewa mwelekeo wa vitendo kwa kusisitiza upandaji wa miti kama ishara ya kuthamini na kulinda mazingira.

Kutokana na ushauri huo, Bodi ya Utalii Tanzania (TTB)leo Januari 27,2026 imeungana na Watanzania wengine kuadhimisha siku hiyo kwa kupanda mti, tendo linalobeba ujumbe wa mazingira ni utu na maendeleo endelevu.

Tukio hilo limeongozwa na Ephraim Mafuru, ambapo mti wa matunda umepandwa kuashiria ukuaji na mafanikio yanayoendelea kushuhudiwa katika sekta ya utalii.

Hatua hiyo inaonesha dhamira ya sekta ya utalii katika kulinda mazingira sambamba na kukuza uchumi, huku ikiweka msingi imara wa urithi chanya kwa vizazi vijavyo.

#MazingiranaUtu #Tanzaniaunforgettable









Na Diana Byera_Bukoba.

Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Mkoa wa Kagera wameungana na Rais Samia Suluhu Hassan kuadhimisha siku yake ya kuzaliwa kwa kupanda miti 2,000 katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Omumwani, Manispaa ya Bukoba.

Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana CCM Mkoa wa Kagera, Faris Buruhani, amewaongoza vijana mbalimbali pamoja na wanafunzi na walimu wa shule hiyo katika zoezi la upandaji miti. Shughuli hiyo pia ilihusisha kukata keki na kuimba nyimbo za kumtakia Rais Samia maisha marefu.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mwenyekiti Buruhani alisema vijana wa Mkoa wa Kagera wanamuunga mkono Rais Samia na wanampongeza kwa kazi kubwa anayoifanya, ikiwemo kudumisha amani na mshikamano, kuimarisha uongozi bora, pamoja na kusimamia miradi mbalimbali inayogusa jamii kwa ustadi.

Amesema shule ya wasichana Omumwani imechaguliwa kama sehemu ya kuwatia moyo wanafunzi kutimiza ndoto zao katika masomo na kujiandaa kupata nyadhifa mbalimbali za kuwatumikia wananchi siku za usoni, pia aliwaasa wanafunzi kulinda miti iliyopandwa na kuhifadhi mazingira.

Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Juliana Rukweto, amevutiwa na uongozi wa mwenyekiti pamoja na mshikamano wa vijana, akisema kuwa hafla hiyo imeacha kumbukumbu ya kudumu, aidha, aliahidi kuendelea kuhamasisha wasichana kusoma kwa bidii na kufanikisha ndoto zao.







 

Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Januari 27, 2026 ameshiriki zoezi la upandaji miti, mbele ya ofisi ya Waziri Mkuu Mlimwa Jijini Dodoma.

Zoezi hilo ni sehemu ya hatua ya kumuunga mkono Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uamuzi wake wa kizalendo wa kuadhimisha siku yake ya kuzaliwa kwa vitendo vya kulinda mazingira. 

Akizungumza baada ya zoezi hilo, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu akiwa ameambatana na mwenza wake Mama Neema Mwigulu, amempongeza Rais Dkt. Samia kwa uongozi wake kwa kuendelea kudhihirisha namna alivyo kiongozi mwenye maono, mbunifu na anayejali maslahi mapana ya Taifa.

“Shughuli hii imekuwa na utofauti kwa kusababisha miti ipandwe kila kona ya nchi, kwenye vitabu vyetu vitukufu, kupanda mti ni moja ya ibada kwasababu wanufaika wa miti ni wengi”

Kadhalika, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu ametoa wito kwa Watanzania kuadhimisha siku zao za kuzaliwa kwa kupanda miti. “Tunapokuwa na jambo la kukumbuka la aina hii, tufanye kitu ambacho kinaweka alama na manufaa kwa watu wengine”.

Mheshimiwa Waziri Mkuu amepanda mtu aina ya MDODOMA/MTIMAJI (Trichilia Emetica).





 

 

Na MASHAKA MHANDO, TANGA.

MKUU wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Balozi Dkt. Batilda Buriani, ameiomba Wizara ya Fedha kuzibana taasisi za fedha zinazotoa mikopo kwa riba kandamizi, huku akitangaza kuanza rasmi kwa utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote mkoani humo ikiwa ni utekelezaji wa ahadi ya Rais ndani ya siku 100 za uongozi wake.

Akifunga kilele cha Wiki ya Huduma za Fedha Kitaifa katika viwanja vya Usagara Jijini Tanga, Dkt. Batilda alitembelea banda la taasisi ya BRAC na kuelezea kusononeshwa na riba kubwa ya asilimia 3.5 kwa mwezi (wastani wa 40% kwa mwaka) wanayotozwa akina mama. 

"Wizara ya Fedha imewaelekeza wakae chini washushe riba hiyo walau ifike asilimia 1.5 ili kuwapunguzia adha akina mama. Tunataka mikopo iwakomboe, siyo iwakandamize," alisema Dkt. Batilda.

Katika hatua nyingine, Dkt. Batilda amewatangazia wakazi wa Tanga kuanza kutolewa kwa vifurushi vya Bima ya Afya kwa Wote, jambo ambalo lilikuwa moja ya kipaumbele na ahadi kuu ya Rais ndani ya siku zake 100 za kwanza madarakani.

Alibainisha kuwa zoezi hilo sasa limeanza rasmi nchini kote, ambapo taasisi mbalimbali za bima ya afya zimeanza kutoa vifurushi hivyo vyenye gharama nafuu ili kuhakikisha kila Mtanzania anapata matibabu bila kikwazo cha fedha.

Alizitaka taasisi za bima kutumia elimu ya fedha waliyoitoa wiki hii kuwahamasisha wananchi kujiunga na vifurushi hivyo sasa.

Mkuu wa Mkoa amezitaka benki za NMB, NBC, na Benki ya Mwalimu kubuni bidhaa zinazogusa wananchi wa chini na kuhakikisha jumuishi la fedha (Financial Inclusion) linafika hadi vijijini.

Dkt. Batilda amewasihi wananchi kutumia wasuluhishi wa migogoro ya fedha walioainishwa na serikali na kujiepusha na mikopo isiyo rasmi inayoweza kuwapotezea mali zao.

Awali akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Kaimu Kamishina wa Idara ya Uendeshaji wa taasisi ya fedha, Dionesia Mjema alibainisha kuwa tangu kuanza kwa Mpango Mkuu wa Maendeleo ya Sekta ya Fedha (2020/21 – 2029/30), Serikali imefanikiwa kutoa elimu kwa jumla ya Watanzania 64,125 katika mikoa 17 nchini.

“Katika idadi hiyo, tumefarijika kuona mwitikio wa wanawake ni mkubwa zaidi, ambapo jumla ya wanawake 41,680 wamefikiwa na elimu hii ikilinganishwa na wanaume 22,445. 

Hii inadhihirisha kuwa nguzo ya uchumi wa familia ambayo ni mwanamke, imeanza kuimarika kitaaluma,” alisema.

Aliongeza kuwa katika kipindi cha kuanzia tarehe 19 hadi 26 Januari 2026, wananchi wa Tanga wamepata fursa ya kipekee ya kujifunza kupitia nyenzo maalum ya Wizara kuhusu usimamizi wa fedha binafsi, uwekezaji katika masoko ya mitaji (hatifungani), bima ya amana, na namna ya kuepuka mikopo yenye masharti kandamizi.

Maadhimisho hayo yaliyobeba kauli mbiu isemayo "Elimu ya Fedha, Msingi wa Maendeleo ya Kiuchumi na Kijamii", yamehusisha taasisi kubwa za fedha nchini zikiwemo Benki Kuu ya Tanzania (BoT), TIRA, CMSA, na wadhamini wakuu kama Benki ya NMB, NBC, Benki ya Biashara ya Mwalimu, UTT-AMIS, na PSSSF.

Akihitimisha alisema mafanikio yaliyopatikana Tanga yanatoa dira kwa Wizara kuendelea kuratibu maadhimisho hayo katika mikoa mingine kila mwaka, kwa lengo la kukuza Pato la Taifa na kuhakikisha kila mwananchi anakuwa na nidhamu ya matumizi ya rasilimali fedha.

Nao baadhi ya wananchi walioshiriki, wakiwemo wavuvi na wajasiriamali wadogo (SMEs), wameishukuru Serikali kwa kuleta huduma hizo karibu, wakisema sasa wanaelewa umuhimu wa kukata bima za vyombo vyao na kuweka akiba kupitia mifuko ya uwekezaji wa pamoja.





Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Dodoma kimeadhimisha siku ya kuzaliwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kukata keki na kupanda miti ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za utunzaji wa mazingira na kuhakikisha Jiji la Dodoma linaendelea kuwa la kijani.

Akizungumza mapema leo, Katibu wa CCM Mkoa wa Dodoma, Pili Mbanga, amesema kuwa maadhimisho hayo yamelenga kuenzi mchango mkubwa wa Rais Samia katika kulinda, kutunza na kuhifadhi mazingira nchini, hususan katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Amesema Dkt. Samia ni mwasisi wa harakati za upandaji miti nchini, akieleza kuwa akiwa Makamu wa Rais alizindua zoezi  la upandaji miti katika eneo la Makutupora mkoani Dodoma, jambo lililoweka msingi wa kampeni za utunzaji wa mazingira zinazoendelea kutekelezwa hadi sasa.

Mbanga ameongeza kuwa CCM Mkoa wa Dodoma imeona ni jambo la muhimu na la heshima kubwa kuadhimisha siku hiyo kwa kupanda miti, kama njia ya kuendeleza maono na mwelekeo wa Rais Samia katika kuhakikisha mazingira yanahifadhiwa kwa faida ya kizazi cha sasa na kijacho.

Ameeleza kuwa upandaji na utunzaji wa miti ni jambo la msingi katika kuboresha mazingira, kusaidia upatikanaji wa mvua, kupunguza athari za joto pamoja na kuboresha mwonekano wa Jiji la Dodoma na maeneo yake ya jirani.

Amehitimisha kwa kuwataka wanachama wa CCM pamoja na wananchi wa Mkoa wa Dodoma kuhakikisha wanashiriki kikamilifu katika kutunza mazingira kwa kupanda na kutunza miti, akisisitiza kuwa mazingira bora ni msingi wa maendeleo ya mkoa na taifa kwa ujumla.







 

Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Mkoa wa Ruvuma limeendelea na zoezi la utoaji wa elimu kwa wateja kwa kuwafikia wanafunzi wa shule za msingi na sekondari  Wilayani Tunduru, kwa lengo la kuwaelimisha kuhusu matumizi sahihi na salama ya umeme majumbani na shuleni.

Katika ziara hiyo, TANESCO imetembelea shule mbalimbali ikiwemo Shule ya Msingi Muungano na Shule ya Sekondari Frankwiston, ambapo Afisa Uhusiano na Huduma kwa Wateja wa shirika hilo, Alan Njiro, amewapatia wanafunzi elimu kuhusu umuhimu wa kutumia umeme kwa uangalifu ili kuepuka madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na matumizi yasiyo sahihi ya nishati hiyo.

Akizungumza na wanafunzi, Njiro amewahimiza kuwasaidia wazazi wao kupunguza gharama za umeme kwa kuzima taa na vifaa vya umeme wanapokuwa hawavitumii, Kwa  kuviondoa kwenye soketi, pamoja na kwenda kuwakumbusha wazazi wao kununua majiko ya umeme na vifaa vya umeme vyinavyotumia umeme kidogo (energy saver) ili kuepuka matumizi ya vifaa vinavyotumia umeme mwingi bila ulazima.

Aidha, wanafunzi wameelimishwa juu ya masuala ya usalama kwa kuonywa kuepuka kuchezea miundombinu ya umeme ikiwemo nyaya zilizo wazi, nguzo na transfoma, huku wakitakiwa kutoa taarifa kwa watu wazima au TANESCO mara moja wanapoona hitilafu yoyote ya umeme katika maeneo yao.

Kwa upande wa uongozi wa shule hizo ulipongeza juhudi za TANESCO Mkoa wa Ruvuma kwa kuwafikia wanafunzi na kuwapatia elimu hiyo muhimu, wakisema itawasaidia kuwa mabalozi wazuri wa matumizi salama na bora ya umeme katika familia na jamii zao kwa ujumla.

Zoezi hili ni sehemu ya mkakati wa TANESCO wa kuimarisha uelewa wa jamii kuhusu matumizi sahihi ya nishati ya umeme, kupunguza gharama kwa wateja na kuongeza usalama, huku shirika likiahidi kuendelea na programu hiyo ya elimu katika shule na maeneo mbalimbali mkoani Ruvuma.



 

-Azindua wa mfumo wa kidigitali wa 'Ongea na Waziri', 

-Asisitiza umuhimu wa uwajibikaji ,utu kwa wahudumu , awataka kuzingatia maadili

Na. Vero Ignatus Arusha

Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa, ametoa maagizo kwa Halmashauri ya Jiji la Arusha kuanza rasmi ujenzi wa jengo la gorofa katika Kituo cha Afya Kaloleni, hatua inayolenga kupunguza msongamano mkubwa wa wagonjwa wanaofika kupata huduma katika kituo hicho.8

Akizungumza hayo Leo Jumatatu Januari 26, 2026 jiji Arusha wakati wa ziara yake ya kukagua utoaji wa huduma za afya katika kituo hicho, Waziri Mchengerwa amesema ongezeko la wagonjwa limefanya miundombinu iliyopo kushindwa kukidhi mahitaji, hivyo ujenzi wa gorofa ni hatua muhimu ya kuboresha huduma na kuongeza ufanisi.

Akizindua wa mfumo wa kidigitali wa 'Ongea na Waziri', Mhe. Mchengerwa amemuagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya afya Dkt. Seif Shekalaghe kuanza mara moja mchakato wa kukipandisha hadhi kituo cha afya Kaloleni ili kuwa Hospitali ya Wilaya, akionesha kuridhishwa na utoaji wa huduma na uwekezaji mkubwa wa Vifaatiba katika Kituo hicho.

Aidha, ametoa maagizo mahsusi kuhakikisha huduma zote za dawa na zinapatikana ndani ya kituo hicho, akisisitiza kuwa hakuna mgonjwa anayepaswa kupelekwa kununua dawa nje ya kituo, kinyume na maelekezo ya serikali na kuhakikisha wananchi wanapata huduma kwa wakati licha ya changamoto zilizopo.

Asiwepo Daktari wa kumuandikia mgonjwa kwenda kununua dawa nje ya hospitali, hatuna changamoto ya dawa MSD inajitosheleza kuleta dawa aina zote, pia nakemea tabia ya baadhi ya na Daktari kuwa na maduka yao ya dawa ambayo mnawaagiza wagonjwa wakanunue dawa, nakuagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya afya Dkt. Seif Shekalaghe zoezi hilo la ufustiliaji lkuanza mara moja. Alisema. 

Waziri Mchengerwa amesisitiza umuhimu wa uwajibikaji na utu kwa wahudumu wa afya, akiwataka kuzingatia maadili ya kazi na kutumia lugha nzuri na yenye staha kwa wagonjwa, kwani huduma bora huanza na mawasiliano mazuri.

Ameongeza kuwa, endapo ujenzi wa kituo hicho cha afya utakamilika kwa wakati na viwango vinavyotakiwa, Serikali itaipandisha hadhi Kituo cha Afya Kaloleni kuwa Hospitali ya Wilaya, kutokana na sifa zake za kuwa na vifaa vya kisasa na uwezo wa kutoa huduma zote muhimu za afya.

"Wizara yake itaendelea kushirikiana pia na Mkoa kuhakikisha huduma za afya zinakuwa bora kwa wananchi, wageni na watalii na kuendana na upekee wa Mkoa wa Arusha katika sekta ya Utalii na ujio wa michuano ya mpira wa miguu ya AFCON 2027' Alisema

Waziri Mchengerwa amesisitiza umuhimu wa uwajibikaji na utu kwa wahudumu wa afya, akiwataka kuzingatia maadili ya kazi na kutumia lugha nzuri na yenye staha kwa wagonjwa, kwani huduma bora huanza na mawasiliano mazuri.

Waziri wa Afya nchini Tanzania Mhe. Mohamed Mchengerwa amesema serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, itajenga Jengo la ghorofa kumi kwenye Hospitali ya Mkoa wa Arusha, Mount Meru, katika jitihada zake za kuimarisha sekta ya afya Mkoani Arusha na kuufanya Mkoa huo kuwa na uwezo zaidi katika kuhudumia wananchi.

Awali katika maelezo yake, Mkuu wa mkoa wa Arusha Mhe. Amos Gabriel Makalla amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uwekezaji huo mkubwa katika sekta ya afya, akiwapongeza na kuahidi kushirikiana na watoa huduma za afya Mkoani hapa katika kutimiza dhamira njema ya Rais Samia katika kuhudumia wananchi wa Mkoa wa Arusha.





 





Na Pamela Mollel, Arusha

Mkoa wa Arusha umefungua ukurasa mpya katika sekta ya afya baada ya kuzinduliwa ujenzi wa Kituo cha Kisasa cha Huduma za Saratani katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Arusha Mount Meru, mradi unaofadhiliwa na kampuni ya Spanish Tiles.

Akizungumza wakati wa uwekaji wa jiwe la msingi la kituo hicho, Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa amesema ujenzi huo ni hatua kubwa itakayobadili maisha ya wagonjwa wa saratani kutoka Arusha na mikoa jirani, waliokuwa wakilazimika kusafiri umbali mrefu kufuata huduma.

Mhe. Mchengerwa ameiagiza Wizara ya Afya kupitia Katibu Mkuu wake Dkt. Seif Shekalaghe kuhakikisha kuwa ndani ya wiki mbili zijazo, vifaa tiba muhimu vinafikishwa hospitalini hapo ili wananchi waanze kupata huduma mara moja.

Ameipongeza kampuni ya Spanish Tiles, chini ya uongozi wa Mkurugenzi Mtendaji Bw. Bobby Chadha, kwa kuonesha uzalendo na moyo wa kuwekeza katika maisha ya Watanzania, akisema mchango huo unaunga mkono juhudi za Serikali katika kusogeza huduma bora za afya karibu na wananchi.

Waziri huyo ametumia fursa hiyo kutoa wito kwa wafanyabiashara na wawekezaji wengine kuiga mfano wa Spanish Tiles kwa kuwekeza kwenye sekta ya afya, akisisitiza kuwa ushirikiano wa sekta binafsi na Serikali ni nguzo muhimu katika kupunguza gharama za matibabu na kuokoa maisha.

Kwa upande wake, Bw. Bobby Chadha ameishukuru Serikali kwa mazingira mazuri ya ushirikiano na kusisitiza kuwa kampuni hiyo imeguswa na wito wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa kuimarisha huduma za afya, hasa katika mikoa inayopokea idadi kubwa ya watalii kama Arusha.

Ameeleza kuwa Spanish Tiles iko tayari kushirikiana zaidi na Serikali katika miradi mingine ya kijamii, hususan kusogeza huduma za saratani katika maeneo mengine yenye uhitaji mkubwa.

Kukamilika kwa kituo hicho kunatarajiwa kupunguza kwa kiasi kikubwa mzigo wa gharama na usumbufu kwa wagonjwa waliokuwa wakilazimika kusafiri hadi Hospitali ya Ocean Road au hata nje ya nchi, hatua itakayoboresha ustawi wa kiuchumi na kijamii wa wananchi.


 Na WAF, Dodoma


Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa ameiasa jamii kuachana na dhana potofu ya kuficha wagonjwa wa Ukoma na kujitokeza wanapobaini viashiria vya ugonjwa huo ili kurahisisha jitihada za Serikali kutokomeza ugonjwa huo nchini.

Waziri Mchengerwa amesema hayo leo Januari 25 2025, wakati alipozungumza na waandishi wa habari akitoa tamko la maadhimisho ya siku ya Ukoma duniani kwenye ofisi za Wizara Jijini Dodoma.

Waziri Mchengerwa amewataka Waganga Wakuu wa Miko ana Wilaya kuhakikisha kaya zote zilizo katika maeneo wanakoibuliwa wagonjwa wapya wa Ukoma zinafuatiliwa na wanakaya wote kufanyiwa uchunguzi na kubaini wenye kuugua Ugonjwa huo na kuwaanzishia matibabu.

“Nichukue fursa hii kuwataka Waganga Wakuu wa Mikoa kuhakikisha kaya zote zilizo katika maeneo wanakoibuliwa Wagonjwa wapya wa Ukoma zinafuatiliwa na wanakaya wote kufanyiwa uchunguzi na kubaini wote wenye kuugua Ugonjwa wa Ukoma na kuwaanzishia matibabu. Tukifanya hivyo kila Mkoa na Halmashauri na kila mahali tunaweza kutokomeza ugonjwa huu hata kabla ya Mwaka 2030,” amesema Mhe. Mchengerwa.

Waziri Mchengerwa ameitaka Mikoa na Halmashauri kuhakikisha wagonjwa wote wanaoibuliwa wanatambuliwa makazi, Kijjji, na Kata anakotoka, ndani ya Wilaya husika au nje ya Mkoa huku akisema iwapo mgonjwa atatokea nje ya Mkoa, ihakikishwe ya kuwa taarifa zake zinapelekwa alikotokea ili kufanya ufuatiliaji na kufanyiwa uchunguzi wa ugonjwa wa Ukoma na kuwapatia tibakinga kaya husika.

Aidha, Mhe. Mchengerwa amesema tangu mwaka 2006, Shirika la Afya Duniani (WHO) limeitangaza Tanzania kuwa tayari imefikia kiwango cha kimataifa cha kutokomeza ugonjwa wa Ukoma cha chini ya mgonjwa mmoja kati ya watu 10,000 ambapo idadi ya wagonjwa wapya wanaogunduliwa nchini inaendelea kupungua kutoka wagonjwa 2,297 mwaka 2015 hadi wagonjwa 1442 mwaka 2025 sawa na punguzo la asilimia 37.

Waziri Mchengerwa amewashukuru watoa huduma katika vituo vya huduma za afya nchini kwa juhudi za kuboresha afya za wananchi na kuhakikisha ugonjwa wa Ukoma unapungua kasi ya kusambaa nchini. Huku akiwapongeza wanahabari kwa kuendelea kuelimisha jamii kuhusu afya bora na namna ya kukabiliana na magonjwa mbalimbali ukiwemo Ugonjwa wa Ukoma.

“Mikoa na halmashauri inabidi mhakikishe kila mgonjwa anayeibuliwa anatambulika anakotoka na taarifa zake zifanyiwe kazi ili kukata mnyororo wa maambukizi, niwashukuru watoa huduma kwa juhudi zenu za kutibia wananchi na wanahabari ambao mnasambaza elimu kwa wananchi juu ya ugonjwa huu,” amesema Mhe. Mchengerwa








Top News