Na Pamela Mollel,Arusha 

Maandalizi ya kuupokea Mwenge wa Uhuru katika Wilaya ya Arusha yamekamilika kwa asilimia 100, huku wananchi wakihimizwa kujitokeza kwa wingi kushiriki katika shughuli za Mbio za Mwenge, kutembelea miradi ya maendeleo na kuhudhuria mkesha mkubwa wa burudani utakaofanyika Viwanja vya FFU Mworombo jijini Arusha 

Akizungumza na waandishi wa habari, Mkuu wa Wilaya ya Arusha, Joseph Mkude, anasema maandalizi yote yamekamilika na wilaya ipo tayari kuupokea Mwenge wa Uhuru, huku akiwataka wananchi kushiriki kikamilifu

Anasema Mwenge wa Uhuru utatembelea na kukagua, kuzindua na kuweka mawe ya msingi katika miradi mbalimbali ya maendeleo, ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha maendeleo na kuhakikisha miradi hiyo inaleta tija kwa wananchi

Mkude anasema mbali na miradi ya maendeleo, Mwenge wa Uhuru utaendelea kuhamasisha wananchi kushiriki katika mapambano dhidi ya UKIMWI, malaria, rushwa, matumizi ya dawa za kulevya na utunzaji wa mazingira kwa kuzingatia kaulimbiu ya mwaka huu isemayo, "Tanzania ni Yetu Sote, Tushikamane kwa Pamoja Kuleta Maendeleo."

Aliongeza kuwa baada ya shughuli za mchana kukamilika, kutafanyika mkesha wa Mwenge wa Uhuru katika Viwanja vya FFU Mworombo, ambapo wananchi watapata burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali wakiongozwa na Ali Kiba na Juma Nature

Aidha, aliwataka wakazi wa Arusha na maeneo ya jirani kutumia fursa hiyo kushuhudia Mbio za Mwenge wa Uhuru, kutembelea miradi ya maendeleo pamoja na kushiriki mkesha huo utakaokuwa na burudani na ujumbe wa uzalendo

Mkude alisema matarajio ya Wilaya ya Arusha ni kuona wananchi wakijitokeza kwa wingi kuupokea Mwenge wa Uhuru na kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo yenye manufaa kwa jamii.



Waziri wa Fedha Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (kushoto), akisikiliza maelezo kutoka kwa mfanyakazi wa NBAA Makyei Ntiro alipotembelea banda la Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) lililopo katika jengo la Wizara ya Fedha katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba).
Waziri wa Fedha Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (kushoto) akipokea zawadi alipotembelea banda la Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA)Happiness Mwamwembe alipotembelea banda la NBAA katika maonesho ya Sabasaba yanayoendelea jijini Dar es Salaam.
Spika wa Bunge Mstaafu, Bi. Anne Makinda (kushoto) akisaini kitabu cha wageni alipotembelea banda la NBAA katika maonesho ya Sabasaba yanayoendelea jijini Dar es Salaam.
Spika wa Bunge Mstaafu, Bi. Anne Makinda (kushoto) akizungumza na watumishi wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) alipotembelea banda la Bodi hiyo lililopo katika jengo la Wizara ya Fedha katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam.
Naibu Waziri wa Fedha Mhe. Laurent Deogratius Luswetula (MB) (kushoto) akizungumza na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya NBAA, CPA. Prof. Sylvia Temu (kulia) alipotembelea banda la Bodi NBAA katika maonesho ya Sabasaba yanayoendelea jijini Dar es Salaam.
Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya NBAA, CPA Dkt. Mwamini Tulli akisikiliza maelezo kutoka kwa mfanyakazi wa NBAA Naimani Fute alipotembelea banda la NBAA katika maonesho ya Sabasaba yanayoendelea jijini Dar es Salaam.(Sabasaba)
Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya NBAA, CPA Dkt. Mwamini Tulli akisaini kitabu alipotembelea banda la NBAA alipotembelea banda la NBAA katika maonesho ya Sabasaba yanayoendelea jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Bw. Dennis Simba akisaini kitabu cha wageni alipotembelea banda la NBAA katika Maonesho ya Sabasaba yanayoendelea jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Bw. Dennis Simba kwenye picha ya pamoja na watumishi wa NBAA alipotembelea banda la Bodi hiyo katika Maonesho ya Sabasaba yanayoendelea jijini Dar es Salaam.
CPA Kulwa Emmanuel Malendeja, Mkurugenzi wa Huduma za Shirika Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA)  akiwa kwenye picha ya pamoja na watumishi wa Bodi hiyo katika Maonesho ya Sabasaba yanayoendelea jijini Dar es Salaam..

Na Mwandishi wetu

Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imesema itaendelea kuweka msukumo katika kuendeleza sayansi na teknolojia kwani ndiyo msingi wa kukuza uchumi kupitia maarifa na kuboresha huduma katika sekta mbalimbali.

Akizungumza  Julai 8, 2026, baada ya kutembelea Taasisi ya Afya na Utafiti ya Ifakara (Ifakara Health Institute-IHI), tawi la Bagamoyo mkoani Pwani, Prof. Mkenda amesema taasisi hiyo ni ya mfano katika tafiti za kisayansi ambazo zinasaidia maendeleo ya sekta ya afya.

Amepongeza kazi za Taasisi hiyo akitolea mfano utafiti chanjo za malaria, majaribio ya dawa (clinical trials) na teknolojia za kisasa zinazotumika  katika utafiti.

Mkenda amesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa IHI na vyuo vikuu vya ndani na vya kimataifa ili kuijengea Tanzania yenye uwezo wa kufanya tafiti zenye viwango vya kimataifa, kuzalisha maarifa na bidhaa zenye manufaa kwa wananchi.

Prof. Mkenda ameongeza kuwa serikali inataka kuona dawa za asili zikifanyiwa utafiti, majaribio ya awali (pre-clinical) na clinical trials ili kuthibitisha ubora na usalama wake  hapa hapa nchini, hatua itakayowezesha Tanzania kuzalisha dawa zilizotokana na gunduzi za ndani na  kunufaika na matokeo yake  kwa kuwa na haki miliki.

Aidha, amesema wizara inaendelea kupitia sera ya Sayansi na Teknolojia ili kuhakikisha inakuwa shirikishi, inatekelezeka na inapimika, sambamba na kuvitaka vyuo vikuu nchini kuweka uzito sawa katika ufundishaji na utafiti.

Akizungumza kwa niaba ya  Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Afya na Utafiti ya Ifakara (Ifakara Health Institute-IHI), tawi la Bagamoyo Dkt Ally Olotu amesema taasisi hiyo immejikita katika kuleta mabadiliko katika mifumo ya afya nchini na nje ya mipaka, kufanya tafiti za chanjo mbalimbali na tabia za jamii kuhusiana na Afya. 









Msemaji Mkuu wa Serikali Gerson Msigwa, ameipongeza Ofisi ya Msajili wa Hazina (OTR) kwa mageuzi inayoendelea kuyasimamia katika taasisi za umma, huku akiitaka kuendeleza juhudi hizo ili kuongeza tija ya uwekezaji wa Serikali.

Msigwa, ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, alitoa pongezi hizo leo, Julai 8, 2026, alipotembelea banda la OTR katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam.

"Hongereni sana kwa mageuzi mnayofanya ambayo yamewezesha kuongezeka kwa gawio na michango mingine kutoka kwa taasisi za umma na kampuni ambazo serikali ina hisa chache. Endeleeni kufanya kazi hiyo kwa bidii zaidi.”

Kwa mwaka wa fedha 2025/26, OTR imekusanya jumla ya Sh1.327 trilioni kutoka katika mashirika ya umma na kampuni ambazo Serikali ina umiliki wa hisa chache.

Kiasi hicho ni ongezeko la takribani Sh300 bilioni ikilinganishwa na Sh1.028 trilioni zilizokusanywa mwaka wa fedha 2024/25, sawa na ukuaji wa asilimia 30.

Aidha, Msigwa aliitaka OTR kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu uwekezaji wa Serikali wenye thamani ya Sh92.3 trilioni unaosimamiwa na Ofisi hiyo, uliowekezwa katika mashirika ya umma na kampuni ambazo Serikali ina hisa chache.

“Wananchi wanapaswa kujua kuwa uwekezaji huu ni mali yao. Hivyo, ni muhimu wauelewe na waulinde kwa maslahi ya Taifa”.

Aliongeza kuwa uelewa wa wananchi kuhusu uwekezaji wa Serikali utasaidia kuongeza uwajibikaji na kuthamini mchango wa taasisi za umma katika maendeleo ya nchi.

Gawio na michango mingine inayokusanywa kutoka kwa mashirika ya umma na kampuni ambazo Serikali ina hisa chache huwasilishwa katika Mfuko Mkuu wa Serikali, ambako hutumika kugharamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo pamoja na utoaji wa huduma muhimu za kijamii, ikiwemo afya na elimu.




 

Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga (Mb), amewataka Watanzania kuendelea kutembelea Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), akisema maonesho ya mwaka huu 2026 yameonesha mafanikio makubwa ya maendeleo ya viwanda, ubunifu wa teknolojia na ubora wa bidhaa zinazozalishwa nchini.

Akizungumza Julai 08, 2026 baada ya kutembelea mabanda mbalimbali ya maonesho hayo, Kapinga amesema mwitikio wa wananchi ni mkubwa kiasi kwamba Serikali inatafakari kuongeza siku moja ya maonesho ili kutoa nafasi kwa wananchi wengi zaidi kushiriki na wafanyabiashara kuendelea kufanya biashara.

Amesema ukubwa wa maonesho hayo unamlazimu kuyatembelea mara kwa mara kwa kuwa haiwezekani kuona mabanda yote kwa siku moja, huku akieleza kuridhishwa na namna waoneshaji walivyojiandaa na ubora wa bidhaa zinazooneshwa.

Waziri Kapinga amesema maonesho ya mwaka 2026 yamebeba teknolojia mbalimbali za kisasa, ikiwemo magari yanayotumia umeme, magari ya mseto (hybrid), magari yanayotumia gesi asilia (CNG) kwa asilimia 100 pamoja na mitambo ya kisasa inayotumia umeme, hatua inayoonesha ukuaji wa sekta ya viwanda na matumizi ya teknolojia rafiki kwa mazingira.

Aidha, amesema bidhaa za ndani zimeendelea kuongezeka ubora, hususan katika thamani na vifungashio, jambo linalodhihirisha mafanikio ya uwekezaji wa Serikali katika kuwawezesha wananchi kiuchumi na kukuza uzalishaji wa ndani.

"Wananchi waendelee kujitokeza kutembelea Sabasaba. Fursa zilizopo mwaka huu ni nyingi zaidi, hivyo ni wakati mzuri wa kujifunza, kufanya biashara na kuona maendeleo ya viwanda vya Tanzania," amesema Kapinga.

Ameongeza kuwa iwapo uamuzi wa kuongeza siku moja ya maonesho utapitishwa, utalenga kuwapa wananchi, hasa wanaokuwa kazini siku za kawaida, nafasi zaidi ya kutembelea maonesho hayo na kunufaika na fursa mbalimbali za biashara na uwekezaji.

Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Juma Zuberi Homera, amewataka watumishi wa sekta ya afya nchini kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi, uadilifu na kuzingatia maadili ya utumishi wa umma ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za afya.

Akizungumza Leo Julai 8,2026 wakati wa uzinduzi wa Kituo cha Afya Kasu kilichopo Kijiji cha Kasu, Kata ya Kandasi, Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi mkoani Rukwa, Dkt. Homera amesema Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaendelea kuwekeza katika kuboresha huduma za afya kwa kujenga na kuboresha miundombinu ya kutolea huduma karibu na wananchi.

Amesema ujenzi wa kituo hicho umegharimu takribani shilingi bilioni 1.8, huku Serikali pia ikipanga kujenga barabara ya kiwango cha lami yenye urefu wa kilomita moja kuelekea kituoni hapo kwa gharama ya takribani shilingi milioni 500, hatua itakayorahisisha upatikanaji wa huduma za afya.

Wananchi wa eneo hilo wameishukuru Serikali kwa kukamilisha mradi huo, wakieleza kuwa utapunguza umbali waliokuwa wakitembea kufuata huduma za afya na kuboresha huduma za mama na mtoto pamoja na huduma nyingine muhimu.




Jane Mwakyoma-Rukwa.

SERIKALI  imetoa siku kumi na nne (14) kwa halmashauri ya wilaya ya Nkasi mkoani Rukwa kuanza kutoa  huduma za matibabu kwa wananchi katika kituo cha Afya Chala .

Akitoa maagizo hayo Waziri wa katiba na sheria Juma Homera baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa kituo cha Afya Chala amesema  baadhi ya mjengo yamekamilika hakuna budi kuanza kufanya kazi na wananchi waendelee kupata huduma katika kituo hicho.

Amesema serikali ya awamu ya sita imejizatiti kuhakikisha huduma za Afya zinatolewa karibu ili kuondoa kero na adha ya kufuata huduma hiyo mbali na makazi ya wananchi.

Aidha Homera ameonya watumishi wa Afya wanaojichukulia fedha kwa wananchi kinyume na taratibu kuacha kuwatoza fedha na badala yake wafanye kazi kwa weledi na kinidhamu na kufuata taratibu zilizowekwa.

Akiwasilisha gharama za ujenzi kwa Waziri wa katiba na sheria Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Nkasi Emmanuel Masaga amesema walipokea fedha sh. 250,000,000 kwaajili ya ujenzi wa jengo la kuhudumia wagonjwa wa nje (OPD), choo cha nje na kichomea taka .

Aidha amesema mradi huo unatekelezwa kwa kutumia mfumo wa FORCE ACCOUNT ambapo mradi huo upo hatua ya umaliziaji na fedha iliyotumika ni shilingi 248,391,255.13 ikiwa fedha iliyobaki shilingi 1,608,744.87 kwaajili ya malipo ya fundi ujenzi.

Pia Masaga amemshukuru Dk.Samia Suluhu Hassan kwa kuwaletea vifaa tiba vyenye thamani ya shilingi 290,669,216.98 katika kituo hicho.

Kwaupande wake diwani wa kata ya Chala Bosco Wazamani amemshukuru Dk. Samia Suluhu Hassan kwa juhudi anazofanya kuhakikisha wananchi wake wanapata huduma bora na za uhakika.

Amesema kujengwa kwa kituo cha Afya katika kata hiyo ni ukombozi tosha kwa wananchi na itakwenda kutatua changamoto ya kutembea umbali mrefu kufuata huduma hiyo.






Kaimu Mkurugenzi mkuu wa Shirika la  Ukaguzi wa Vyama vya Ushirika COASCO, CPA Jeremiah Mugeta, amesema Kilimo kinamchango mkubwa katika uchumi wa nchi, kwa mujibu wa Takwimu zilizopo zinaonyesha kwamba kilimo pekee kinachangia zaidi ya asilimia 26 katika pato la Taifa, jambo ambalo ni kubwa na lakujivunia na kuona namna ambavyo ushirika unachangia kwenye maendeleo ya uchumi.

Akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), Julai 8, 2026, Mugeta amesema mchango wa sekta ya ushirika katika maendeleo ya uchumi ni mkubwa, ambapo mazao yanayouzwa kupitia vyama vya ushirika huchangia zaidi ya dola za Marekani bilioni 2 kwa mwaka, jambo linaloonesha umuhimu wa ushirika katika kukuza uchumi wa nchi.

Akizungumzia suala la ukaguzi wa vyama vya ushirika amesema wamejipanga kuhakikisha ushirika unazidi kuwa imara, na wauhakika huku malengo Yao na mipango Yao ni kuhakikisha wanaushirika wanapata elimu bora pamoja na misingi na kanuni na taratibu za kuendesha vyama vya ushirika, 

Aidha CASCO kila mwaka huwa wanaandaa taarifa ya jumla ya kuonyesha matokeo ya jinsi ambavyo vyama vya ushirika vilivyofanya shughuli zake kila mwaka, na kutoa maoni katika ukaguzi wanaoufanya.

Vilevile amebainisha mpango walionao katika mwaka wa fedha 2026/2027, wamejipanga kuhakikisha vyama vyote vya ushirika vinakaguliwa ili kuweza kuwapa fursa wanaushirika kujua maendeleo ya shughuli wanazofanya kwenye vyama hivyo, 

Ameeleza mkakati uliopo ni kushirikiana na Tume ya maendeleo ya ushirika, kuhakikisha vyama na viongozi wa vyama vya ushirika wanapata taarifa Sahihi ya watu gani watakaguliwa na ukaguzi huo unatarajiwa kuanza mwezi huu wa Julai kuanzia tarehe 20.

Ametoa wito kwa wanaushirika ni kuhakikisha wanaandaa taarifa za fedha za mwaka 2025/2026 na kuziwasilisha katika ofisi za COASCO zilizopo kwenye mikoa Yao ili ukaguzi uwafikie kwa wakati,  na wahakikishe wanazingatia sheria na kanuni za kuandaa taarifa za fedha ili kupunguza hati chafu katika ukaguzi.







Na Mwandishi Wetu.

Zanzibar. Equity Group, kwa kushirikiana na Mamlaka ya Kukuza Uwekezaji Zanzibar (ZIPA), imeongoza ujumbe wa viongozi na wadau kutoka Tanzania Bara na Zanzibar kutembelea mradi wa Bandari ya Fumba, hatua inayolenga kuhamasisha uwekezaji na kuonyesha fursa za maendeleo ya kiuchumi zilizopo visiwani humo.

Ziara hiyo ni sehemu ya juhudi za kuwaleta pamoja wawekezaji na taasisi za Serikali ili kuimarisha mazingira ya biashara na kuongeza uwekezaji katika miradi ya kimkakati itakayochochea ukuaji wa uchumi.

Equity Bank, ambayo ni mmoja wa wafadhili wakuu wa mradi wa Bandari ya Fumba, imesema itaendelea kuunga mkono uwekezaji katika miundombinu yenye uwezo wa kuchochea biashara, kuongeza ajira na kuimarisha ushindani wa Zanzibar na Tanzania katika soko la kikanda na kimataifa.

Benki hiyo imeeleza kuwa dhamira yake inaenda zaidi ya utoaji wa huduma za kifedha, kwa kuwezesha ushirikiano kati ya wawekezaji wa ndani na wa kimataifa pamoja na mamlaka za udhibiti ili kujenga mazingira rafiki ya uwekezaji.

Aidha, juhudi hizo zinaunga mkono utekelezaji wa Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA), kwa lengo la kuimarisha biashara ya kikanda, kuvutia mitaji mipya na kufungua fursa zaidi za maendeleo ya uchumi endelevu nchini Tanzania na barani Afrika.


OFISA Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) CPA. Nicodemus Mkama amesema mafanikio ya asilimia 760.78, yameifanya Hatifungani ya iTrust kuweka historia ya kuwa Hatifungani iliyopata mafanikio makubwa zaidi kupita hatifungani zote zilizowahi kutolewa hapa nchini. 

Amesema hatifungani iliyokuwa inashikilia rekodi hiyo, ni Hatifungani ya kampuni ya First Housing Finance Limited yaani MAKAZI Bond ambayo ilipata mafanikio ya asilimia 661.1 na kuorodheshwa kwenye Soko la Hisa tarehe 09 Juni 2026 huku akiipongeza iTrust kwa kuvunja rekodi na kuendelea kuweka rekodi za mafanikio katika masoko ya mitaji.

CPA.Mkama ameyasema hayo leo Julai 8,2026 jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya kuorodheshwa kwa Hatifungani ya Kampuni ya iTRUST Finance Limited katika Soka la Hisa Dar es Salaam 

“Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) pamoja na wadau wote wa sekta ya masoko ya mitaji tumefurahishwa sana na hatua hii, na tunatoa pongezi za dhati kwa Bodi na Menejimenti ya iTrust Finance Limited, wataalamu wote waliohusika kwa kuweka rekodi hii ya kihistoria.”

Amesema iTrust Finance Limited imeendelea kuwa mfano bora na wa kuigwa kwa kampuni na taasisi katika sekta ya umma na binafsi, kwani kampuni hiyo imekuwa ikitumia vizuri fursa zinazopatikana katika masoko ya mitaji kupata rasilimali fedha za kukuza na kuendeleza biashara; kuimarisha utendaji wa Kampuni; na kugharamia shughuli za maendeleo.

“Tangu mwaka 2021 (wakati huo kampuni hii ikitumia jina la Imaan Finance Limited) na hadi hivi sasa ikiwa na jina la iTrust Finance Limited, Kampuni hii imetumia fursa za masoko ya mitaji kwa njia ya utoaji wa Hatifungani, Sukuk na Mifuko ya Uwekezaji wa Pamoja.

Akifafanua zaidi amesema hatifungani hiyo ni ya kipekee na muhimu katika maendeleo na ustawi wa masoko ya mitaji, sio tu Tanzania, bali katika ukanda wa Afrika Mashariki, kwani hatifungani hii inaweka historia na rekodi kuu Tatu,

Amesema ni hatifungani ya kwanza (1) kuorodheshwa kwenye Soko la Hisa la Dar es Salaam, ikiwa imetolewa na kampuni yenye Leseni ya Uwakala wa Soko la Hisa (Licensed Broker/Dealer); na Leseni ya Usimamizi wa Mifuko ya Uwekezaji (Fund Manager) iliyotolewa na CMSA.

Pia ni hatifungani ambayo mauzo ya toleo la kwanza yameweza kuzidi kiasi cha Programu nzima ya Hatifungani yenye Thamani ya shilingi bilioni 100 zilizokuwa zitolewe katika awamu nne ndani ya miaka minne (bilioni 15, 20, 30 na 35, katika mwaka 2026, 2027, 2028 na 2029 mtawalia).

“Kama tulivyoshuhudia mauzo ya Hatifungani ya iTrust yamepata mafanikio ya asilimia 760.78, ambapo kiasi cha shilingi bilioni 114.12 kimepatikana, ikilinganishwa na shilingi bilioni 15 zilizotarajiwa,”amesema.

Akieleza zaidi amesema mojawapo ya malengo ya DIRA ya Taifa ya Maendeleo (DIRA 2050) ni kuona kuwa Sekta ya Fedha, inawezesha upatikanaji wa rasilimali fedha kwa ajili ya kukuza na kuendeleza biashara ambazo zinachangia ukuaji na ustawi wa sekta binafsi;

sekta ya umma na uchumi wa nchi kwa ujumla hapa nchini. 

“Hivyo basi, juhudi za iTrust Finance Limited zinatoa mchango katika utekelezaji wa malengo haya, na ni hatua madhubuti ya kuongeza fursa za uwekezaji katika masoko ya mitaji na kuleta matokeo chanya kwenye uchumi wa nchi yetu.”

Pia amesema kati ya wawekezaji waliowekeza kwenye hatifungani ya iTrust, asilimia 66.66 ni wawekezaji mmoja mmoja yaani Retail Investors na asilimia 33.34 ni Kampuni na Taasisi yaani Institutional investors . 

Aidha, asilimia 98.82 ni wawekezaji wa ndani na asilimia 1.18 ni wawekezaji wa kigeni huku akifafanua kuorodheshwa kwa hatifungani hiyo kunaongeza thamani ya uwekezaji katika Hatifungani za Kampuni na Taasisi kwa asilimia 5.46 na kufikia shilingi trilioni 2.20, kutoka shilingi trilioni 2.09. 

“Ushiriki mkubwa wa wawekezaji mmoja mmoja wa ndani ni hatua muhimu katika kuongeza ukwasi (liquidity) katika soko la hisa. Aidha, hii sehemu muhimu ya utekelezaji wa Mpango Jumuishi wa Huduma za Kifedha yaani National

Financial Inclusion Framework wenye lengo la kuongeza ushiriki wa wananchi kwenye sekta rasmi ya fedha.

“Takribani asilimia 89 ya maombi yote ya uwekezaji kwenye Hatifungani ya iTrust

yamefanyika na kupokelewa kupitia mifumo ya kidijitali, ambapo mfumo wa kidijitali wa iTrust App pekee umechangia zaidi ya asilimia 71 ya maombi yote.”

CPA.Mkama amesema mafanikio hayo ni uthibitisho wa imani ya waliyonayo wawekezaji kwa Kampuni ya iTrust Finance Limited na masoko ya mitaji nchini. Aidha, mafanikio hayo ni matokeo ya mazingira wezeshi ya kisera, kisheria na kiutendaji yanayotolewa na Serikali katika masoko ya mitaji. 





Top News