Mkurugenzi wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB), Bw. Asangye Bangu, amewataka waendesha maghala kuzingatia uadilifu, uwajibikaji na utoaji wa huduma bora ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala.

Akifungua kikao maalumu cha waendesha maghala kilichofanyika mjini Morogoro Julai 1, 2026, Bangu, amesema waendesha ghala wanapaswa kuendana na wakati kwa kuwa waadilifu, kutoa huduma zenye viwango vya juu na kuhakikisha mfumo wa stakabadhi za ghala unaendelea kuwa na tija kwa wakulima, wafanyabiashara na wananchi kwa ujumla.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Waendesha ghala Tanzania, Abdulikarim amesema kikao hicho kimeandaliwa kwa lengo la kuongeza uelewa kuhusu masuala mbalimbali ya kiutendaji, kujadili changamoto zinazowakabili pamoja na kutafuta suluhisho la kuboresha maslahi ya waendesha ghala kutokana na kupanda kwa gharama za maisha na uendeshaji wa shughuli zao.

Ameongeza kuwa maazimio na maelekezo yaliyotolewa katika kikao hicho yatawasaidia waendesha ghala kuongeza ufanisi wa kazi zao na kuendelea kutoa huduma bora kwa wadau wote wa sekta ya kilimo.
Mkurugenzi wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB), Bw. Asangye Bangu, amekutana na kufanya mazungumzo na Afisa Biashara kutoka Ubalozi wa Misri nchini Tanzania, Bw. Wael Aref, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa kibiashara kupitia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala ili kupanua masoko ya mazao na mifugo kati ya nchi hizo mbili.

Mazungumzo hayo yamefanyika leo Julai 2, 2026 jijini Dar es Salaam ambapo Bw. Bangu ameelezea majukumu ya WRRB pamoja na namna Mfumo wa Stakabadhi za Ghala unavyowawezesha wakulima na wazalishaji kupata masoko yenye ushindani, kuongeza thamani ya mazao yao, na kuunganishwa moja kwa moja na wanunuzi wa ndani na nje ya nchi.

Amesema mfumo huo umeendelea kuwa nyenzo muhimu katika sekta ya kilimo kwa kuweka mazingira ya uwazi, kuongeza ushindani wa bei, na kuhakikisha wazalishaji wanapata uhakika wa masoko yao.

Aidha, viongozi hao wamejadili pia uwezekano wa kupanua wigo wa ushirikiano huo kwa kuingiza mifugo hai katika Mfumo wa Stakabadhi za Ghala ili kuongeza aina ya bidhaa zinazoweza kuuzwa kupitia mfumo huo na kufungua fursa mpya za biashara kati ya Tanzania na Misri.
-Asema mijadala iko huru kwa wabunge wa vyama vyote, aeleza wapinzani wanavyopewa nafasi

-Pia azungumzia maandalizi kuelekea historia miaka 100 ya Bunge la Jamhuri ya Muungano




Na Said Mwishehe,Michuzi TV


SPIKA wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mussa Azzan Zungu, amevunja ukimya huku akiwazodoa wale wanadai Bunge ni dhaifu na halina meno.

Kutokana na hali hiyo, amesema kuwa Bunge lililopo na yake yaliyopita hakuna lililo dhaifu kwani kazi kubwa inayofanyika ni kuisimamia Serikali pamoja na kuwawakilisha wananchi ikiwamo kutunga sheria mbalimbali pamoja na kusimamia ustawi wa jamii.

Akizungumza katika kikao kati yake na wahariri wa vyombo vya habari kuhusu miaka 100 ya historia ya Bunge, ametumia nafasi hiyo kueleza kuwa nyakati zote likiwamo Bunge analoliongoza bado anatoa uwanja sawa kwa wabunge wa upinzani picha ya uchache wao.

Aidha amesema na kuhoji kuwa mjadala wa Bunge kuonekana dhaifu lakini nyakati zote bado wabunge wa upinzani wamekuwa wakipewa haki sawa kama takwa la kidemokrasia linavyotaka.

“Ndugu zangu kuna mambo yanaendelea na kuibuliwa na baadhi ya vyama vya upinzani. Kumbukeni mwaka 2015 Katiba ilikuwa ileile ambapo wabunge wa upinzani walikuwa 102 ambapo kati ya hao Chadema walikuwa 69.

“Tena wakati wanashinda Tume ya Uchaguzi kwa wakati ule haikuwa na maboresho na kambi rasmi ya upinzani ikatambulika.

“… kwanini Bunge lile lilikuwa na nguvu, lakini nini maana yake mjadala hapa chama kimoja (hakutaja jina) chama kimoja kilipata mgombea toka CCM katika uchaguzi wa mwaka 2015 jambo lililowasaidia kuimarika zaidi na kupata wabunge wengi. Sasa wapo wapinzani lakini hawajaimarika.

“Hapa Dar es Salaam wapinzani waliweza kuongoza Halmashauri za Kinondoni, Ubungo na hata Ilala pia ambazo zilikuwa upinzani na hata kufikia baadhi yao kusema wapewe nafasi ili tuongoze,” amesema Spika Bunge

Ameongeza kazi ya Bunge ambayo inafanyika kwa miaka yote kwanza kuisimamia ustawi wa wananchi, kuisimamia Serikali pamoja na kitunga sheria jambo ambalo linaendelea kufanyika hadi sasa.

Katika kujenga hoja yake kuhusu Bunge analoliongoza alisisitiza kuwa hakuna Bunge dhaifu au Bunge imara kwani Bunge lolote kazi zake zinajulikana kusimamia ustawi wa jamii.


KAMATI SAA 72 BUNGENI


Spika Zungu amesema kutokana na kutoa haki kwa wabunge na wananchi baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 vyama vyote vya upinzani vimeweza kupata wabunge tisa wakati hata ukitoa hoja ili uungwe mkono lazima muwe wabunge 10 lakini upinzani wakisimama wanakuwa tisa.

“Zipo hoja nzuri huyu hapa Ado (Mbunge wa Tunduru ACT) hata akitoa hoja wanakuwa tisa wakati kanuni inataka wawe 10,” amesema.

Amefafanua licha ya hali hiyo na takwa la kikanuni lakini bado Rais Samia aliagiza kamati za Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Serikali za Mitaa (LAAC) ziongozwe na wapinzani licha ya uchache wao kama njia ya kuimarisha demokrasia.

“Ni nani asiyejua kwamba Rais Dkt Samia ndio amewarudisha nchini wapinzani wengine waliokimbia nchi kwa kuwataka warudi ili tujenge Taifa letu, haya ni mapenzi makubwa ya Rais Samia.

“Hata mnaposikia ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali lakini kamati ambayo kwenye Mpira tunaita kamati ya saa 72 Kwa maana PAC na LAAC ndio wajibu wa kumwita kila aliyetajwa,” amesema.



MIAKA 100 YA BUNGE


Amesema kwa sasa Bunge lipo kwenye maandalizi ya kusheherekea miaka 100 tangu kilipoanzishwa chombo hicho wakati wa utawala wa ukoloni hadi ilipozaliwa Tanzania.

“Wapo wengine watahoji kwa nini tunawataja wakoloni lazima tuwataje ili tuone tulipotoka, tulipo na tunapokwenda.

“Kauli mbiu yetu katika kutimiza miaka 100 ya Bunge ni Historia yetu,Dira yetu,” amesema Spika Zungu.












Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), Siasa na Mahusiano ya Kimataifa wa CCM, Rabia Hamid, amefanya ziara leo 2 Julai katika Mikoa ya Manyara na Kilimanjaro. 

Akiwa mkoani Manyara, Rabia alipokelewa na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Manyara, Ndugu Petter Toima, kabla ya kushiriki kikao cha Kamati ya Siasa na Halmashauri kuu ya Mkoa, ambapo aliwataka wajumbe kuendelea kuimarisha umoja na ushirikiano katika kutekeleza majukumu ya chama pamoja na kusimamia kwa ufanisi miradi ya CCM.

“Wajumbe wa Kamati ya Siasa tuwe na umoja na ushirikiano katika kuimarisha chama na kusimamia miradi pamoja na kutekeleza maelekezo ya chama. Tuache siasa za makundi,” alisema Rabia.

Baada ya kumaliza ziara yake mkoani Manyara, Rabia aliendelea na ziara ya ulezi mkoani Kilimanjaro ambako alishiriki kikao cha Kamati ya Siasa ya Mkoa na kupokelewa na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kilimanjaro, Patrick Boisafi.

“ Umoja na amani ni msingi wa mafanikio ya chama chetu. wajumbe tuendelee kudumisha umoja, mshikamano na amani tushirikiane, tuheshimiane na tuendelee kutekeleza majukumu yetu kwa maslahi ya chama na Taifa,” alisema katika kikao cha Kamati ya siasa na Halmashauri kuu ya Mkoa Kilimanjaro.

Ziara ya Rabia katika mikoa ya Manyara na Kilimanjaro ni sehemu ya utekelezaji wa majukumu yake ya ulezi yenye lengo la kuimarisha uhai wa chama, kufuatilia utekelezaji wa maelekezo ya chama na kusikiliza maendeleo ya shughuli mbalimbali katika mikoa hiyo.

















Top News