Wafugaji nchini wameendelea kunufaika na huduma za kifedha baada ya kuongezeka kwa uelewa wao kuhusu masuala ya fedha na uwekezaji, hatua iliyowezesha kurahisishwa kwa vigezo vya dhamana ya kupata mikopo  kwa kutumia rasilimali walizonazo.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa Maonyesho ya Mifugo Kanda ya Ziwa, Meneja Biashara wa Benki ya CRDB Kanda ya Magharibi, Anselem Mwenda, amesema benki hiyo imefanikiwa kuwasaidia wafugaji wengi kupata mikopo kwa urahisi kupitia huduma mbalimbali ikiwemo bima ya mifugo.

Mwenda alitoa kauli hiyo mara baada ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Agnes Meena, kutembelea banda la CRDB, ambao ni wadhamini wakuu wa maonyesho hayo.

Alisema kuwa kwa sasa wafugaji wana uwezo wa kukopesheka kwa urahisi zaidi kutokana na kuwa na bima ya mifugo pamoja na kutambuliwa kwa rasilimali zao kama sehemu ya dhamana.

“Uelewa wa wafugaji umeongezeka kwa kiwango kikubwa tofauti na ilivyokuwa zamani. Hii imewasaidia kutumia fursa za kifedha zinazotolewa na benki kwa maendeleo ya shughuli zao."

Aliongeza kuwa huduma zote za kibenki zinaendelea kutolewa katika banda la CRDB kwa kipindi cha siku mbili za maonyesho hayo, kuanzia Mei 30 hadi 31, huku akiwakaribisha wafugaji na wadau wengine kufika kupata huduma pamoja na elimu ya masuala ya fedha.

Mwenda alisisitiza umuhimu wa wafugaji kuendelea kujifunza kuhusu usimamizi wa fedha na matumizi sahihi ya mikopo ili kuongeza tija katika sekta ya mifugo na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.



 

Wafugaji nchini wametakiwa kuachana na mbinu za jadi za ufugaji ambazo zimepitwa na wakati na badala yake kutumia teknolojia za kisasa za kidigitali zinazorahisisha usimamizi na ufuatiliaji wa mifugo kuanzia inapozaliwa hadi hatua ya kuchinjwa.

Wito huo umetolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Climb Up Limited, Emmanuel Ngallah, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika Maonyesho ya Mifugo Kanda ya Ziwa Mei 30, 2026, mkoani Shinyanga.

Ngallah alisema matumizi ya mifumo ya kidigitali katika sekta ya mifugo yanawawezesha wafugaji kupata taarifa sahihi kuhusu afya, ukuaji na historia ya mifugo yao, jambo linaloongeza tija na thamani ya biashara ya mifugo.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Agnes Meena mgeni rasmi katika maonyesho hayo, alisisitiza umuhimu wa wafugaji kuendana na mabadiliko ya teknolojia ili kuongeza uzalishaji na kuifanya sekta ya mifugo kuwa na mchango mkubwa zaidi katika uchumi wa nchi.

Alieleza kuwa serikali inaendelea kuhamasisha matumizi ya teknolojia katika ufugaji ili kuboresha usimamizi wa mifugo, kuongeza ubora wa bidhaa zinazotokana na mifugo na kufungua fursa zaidi za masoko ya ndani na nje ya nchi.

Wakati huo huo, baadhi ya wananchi waliotembelea banda la Climb Up Limited katika maonesho hayo wameeleza kufurahishwa na elimu waliyoipata kuhusu ufugaji wa kisasa na matumizi ya mifumo ya kidigitali.

Wamesema maarifa hayo yatawasaidia kuboresha shughuli zao za ufugaji, kuongeza uzalishaji na kufuatilia kwa urahisi maendeleo ya mifugo yao kwa kutumia teknolojia.

Maonesho ya Mifugo Kanda ya Ziwa yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kuwakutanisha wadau wa sekta ya mifugo, kampuni za teknolojia na wafugaji kwa lengo la kubadilishana uzoefu na kuhamasisha matumizi ya mbinu za kisasa katika uzalishaji wa mifugo.





 


Na  MWANDISHI WETU

DIWANI wa Kata ya kisutu, jijini Dar es Salaam, kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi CCM)  , Tousif Bhojani, ameibua shangwe kwa wakazi wa eneo hilo baada ya kuzipatia ufumbuzi kero mbalimbali  zilizo kuwa zikiwakabili.

Bhojani  ametatua karo mbalimbali  za wananchi katika mkutano wa hadhara  wa kusikiliza na kutatua kero  uliofanyika katika Viwanja vya Soko la Kisutu, ambao ulihusisha pia  wataalamu kutoka taasisi mbalimbali za serikali ambao walizitolea majibu baadhi ya  changamoto.

Kero hizo ni pamoja na ukosefu wa kisima cha maji katika Soko la Baba na Mamalishe Kisutu, kuvuja kwa paa la soko hilo na ukosefu wa vifaa vya zimamoto.

Changamoto zingine ni maegesho, kero ya kamata kamata ya  'wrong parking', ulinzi na usalama, mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri na  utirikaji wa maji taka.

Katika kutatua  changamoto ya Soko la Mama na Baba Lishe Kisutu kutokuwa na kisima, Diwani Bhojani aliwasiliana kwa simu papo hapo   na Spika wa Bunge  ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Ilala, Mussa Hassan Zungu, ambaye  aliwahutubia wananchi kwa njia ya simu na kuahidi kushirikiana na diwani huyo kutatua kero hiyo.

Akizungumza kwa njia ya simu Spika Zungu amewataka wananchi kushikamana, kuwa wamoja na kuahidi kero mbalimbali  kuwa zitatuliwa kwa kushirikiana na diwani wao huyo, jambo lililozua shangwe.

"Baada ya kukata simu Spika na Mbunge wetu Zungu, amenitumia ujumbe kuwa tutahakikisha kisima cha maji kina jengwa hapa.Kuhusu paa  la soko kuvuja  nimewasiliana hapa hapa na Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam, Elihuruma Mabelya, ameahidi kuja mwenyewe  kukagua na kuna kushughulikia kero hiyo,"amesema Diwani Bhojani.

Diwani huyo pia ameahidi kutoa kifaa cha kuzimia moto katika soko hilo mapema wiki ijayo.

Kuhusu changamoto ya ubovu wa barabara kutokana mvua iliyonyesha, Diwani Bhojani ameahidi kuiwasilisha kwa Wakala wa Barabara Mjini na Vijijini (TARURA) ili kurekebishwa.

Akizungumzia ulinzi na usalama, diwani huyo amesema kuna vikundoi vya sungusungu v kwa kushirikiana na Jeshi la polisi, vinaimarisha ulinzi katika kata hiyo hivyo kuwatoa hofu na kuwataka kuchangia  ada ya ulinzi. 

Changamoto zingine zilijibiwa na  taasisi za serikali hususan  Jeshi la Zimamoto na Ukoaji, ambalo liliahidi kufanya ukaguzi katika soko hilo.

Kwa upande wa kero  ya maji  Mwakilishi wa Mamlaka ya Majisafi na  Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) amewatoa wasaiwasi wananchi kuhusu upatikanaji wa maji kwamba mamlaka hiyo  inaendelea kuimarisha mifumo yake kuhakikisha maji yanapatikana wakati wote.

Kuhusu mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na Halmashauri ya Jiji la Dar es  Salaam,  mwakilishi kutoka jiji hilo, amesema kata hiyo imenufaika na mikopo  ya jumla ya sh. milioni 169 ambazo zimetolewa kwa vikundi vitano, hivyo kuwataka wananchi kuunda vikundi  kwani mikopo hiyo ipo na inaendelea kutolewa.

Wananchi wa kata hiyo wamempongeza Diwani Bhojani kwa utaratibu wa kuandaa mikutano na kusikiliza kero zao  kwani ni njia rahisi ya kutatua kero hizo kabla hazijaleta adha kubwa.









 

 

Na Hassan Kimweri, WAF - Kagera 

Tanzania imeendelea kuimarisha udhibiti dhidi ya ugonjwa wa Ebola kwa kushirikiana na nchi jirani ikiwemo Uganda, Rwanda, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Burundi na Kenya kupitia  ushirikiano wa kikanda ili kudhibiti kusambaa kwa maambukizi ya Ebola.

Mganga Mkuu wa Serikali Dkt. Grace Magembe amesema Hayo leo Mei 30, 2026 akiwa katika ziara mkoani Kagera kwa lengo la kukagua udhibiti na utayari wa kukabiliana na ugonjwa huo mipakani pamoja na vituo vya afya vya kutolea huduma za dharula akiambatana na timu kutoka Wizara ya Afya, OWM- TAMISEMI na Mkoa wa Kagera. 

"Zaidi ya wasafiri elfu 75,000 wamefanyiwa uchunguzi katika mipaka mbalimbali nchini tangu kuongezeka kwa tahadhari za Ebola, huku takribani watu 45,000 wakifanyiwa tathmini ya kina zaidi kutokana na kuhisiwa lakini hakuna aliyebainika na ugonjwa wa Ebola," amesema Dkt. Magembe

Amesema, Serikali imeweka mifumo ya ufuatiliaji katika mipaka yote ya nchi ikiwemo mipaka ya nchi kavu, viwanja vya ndege, bandari na maeneo mengine ya kuvukia, ambapo wasafiri wote wanaingia nchini hupimwa na kufanyiwa uchunguzi wa afya.

Aidha, Dkt. Magembe amesema kuwa wahisiwa hao walitambuliwa kwa kuzingatia vigezo vya kitaalamu vya uchunguzi wa Ebola vya kitaifa na kimataifa kama inavyoelekezwa na Shirika la Afya Duniani (WHO) ikiwemo historia ya kusafiri kutoka maeneo yenye maambukizi, kuwasiliana na watu wenye dalili zinazofanana na Ebola au kuwa na baadhi ya dalili zinazohusishwa na ugonjwa huo.

“Tumefanya vipimo na uchunguzi kwa watu wote waliotiliwa shaka, lakini hadi sasa hakuna hata mtu mmoja aliyebainika kuwa na maambukizi ya ugonjwa wa Ebola nchini Tanzania,” amesema Dkt. Magembe.

Amefafanua kuwa dalili za Ebola zinaweza kufanana na magonjwa mengine , hivyo amewataka wataalamu wa afya katika vituo vya kutolea huduma kuendelea kuwahoji na kuwachunguza wagonjwa wote wenye dalili zinazoweza kuashiria magonjwa ya mlipuko huku wakichukua tahadhari zote muhimu kujikinga ili wasipate maambukizi.

Mwisho, Dkt. Magembe amewataka wananchi kuendelea kutoa taarifa kupitia namba ya dharura 199 , ofisi za serikali za vijiji na mitaa na  vituo vya afya vilivyo karibu nao pindi wanapobaini mtu mwenye dalili zinazotia shaka, akisisitiza kuwa watumishi wa afya wanaendelea kufanya kazi usiku na mchana kuhakikisha Tanzania inaendelea kuwa salama dhidi ya ugonjwa wa Ebola.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa huduma za Kinga Wizara ya Afya Dkt. Otilia Gowelle amesema mwananchi yeyote anaefika katika kituo cha kutolea huduma anapata elimu sahihi ya namna ya kujikinga na ugonjwa huo ikiwemo kutoa elimu kupitia TV, vipeperushi pamoja na watoa huduma za afya.











📍 Ni zile familia 67 zilizobomolewa nyumba na Amboni Plantation 

Na Mwandishi Wetu, Kigombe

MBUNGE wa Muheza, Mhe. Hamis Mwinjuma (MwanaFA), amewahakikishia wananchi wa kaya 67 waliobomolewa nyumba zao na Kampuni ya Amboni Plantation kuwa watalipwa fidia zao kikamilifu.

Uharibifu huo wa dharura ulioacha familia hizo za Kitongoji cha Maisha Plus mkoani Tanga zikilala nje, ulifanyika mwishoni mwa wiki iliyopita kwa madai ya wananchi hao kuvamia eneo la shamba la mkonge la mwekezaji huyo.

Akizungumza jana Mei 29, 2026 aliporejea kijijini hapo kutoa mrejesho wa kikao chake cha ndani na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dkt. Batilda Burian, MwanaFA alisema Serikali imejipanga vizuri kulinda utu wa wanyonge hao.

"Sitaki kuwaambia ni kiasi gani mtalipwa, lakini sisi kama viongozi wenu tunawahakikishia jambo lenu litakwenda vizuri na mtalipwa fidia kabla ya kuondoka hapa. Suala hili linanikosesha usingizi na sitarudi kwenye majukumu ya kitaifa hadi dharura hii iishe," alisema MwanaFA.

Mbunge huyo, ambaye pia ni Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, alisema ameshazungumza na taasisi zinazosimamia majanga nchini ili kuleta mahema ya kisasa yatakayotumika kama makazi ya muda ya dharura kujikinga na mvua za mchoo.

Kuhusu mchakato wa kisheria, Mhe. Mwinjuma alibainisha kuwa Mkuu wa Mkoa anaunda Tume Maalum kupitia upya hukumu ya kesi hiyo na namna ubomoaji ulivyotekelezwa.

Maazimio mengine ya dharura yaliyofikiwa ni pamoja na kuwataka waliohusika na ubomoaji huo kuwajibishwa kwa kufanya oparesheni bila taarifa kwa Serikali, kumlazimisha mwekezaji asafishe eneo jipya, kuwapa wananchi hati, na kutoa fedha za "kifuta machozi".

Hata hivyo, wananchi wa eneo hilo wametoa kasoro mpango wa kuhamishiwa kwenye ardhi mpya yenye ekari 37 iliyotolewa na mwekezaji, wakidai haina sifa za makazi ya binadamu.

Mwananchi Ernest John, alitahadharisha kuwa eneo hilo ni mkondo wa asili wa njia za maji, huku Hamad Hamza akibainisha kuwa limefichama porini na halina huduma za msingi.

"Huko tunakopelekwa ni porini, hakuna shule wala zahanati. Tunaomba Serikali ituchagulie maeneo ya kwenda kukaa, lakini yawe karibu na vijiji vya Pangani kule Kimang'a au Kwasawaka ili watoto wetu wapate huduma, na sio kututupa kwenye hatari ya mafuriko kwa maelekezo ya mwekezaji," alilalamika mkazi Jane Sekela Msigalo.

Mhe. Mwinjuma alituliza mzuka na kuahidi kuwa wataalamu wa ardhi na mazingira watafanya vipimo vya kitalamu vya udongo kwanza, na kama eneo hilo lina changamoto ya maji halitotumika.

Katika mkutano huo, Diwani wa Kata ya Kigombe, Mhe. Shahongwe Mgandi, alimshukuru Mkuu wa Mkoa kwa kupeleka kitoweo cha ng'ombe wa sikukuu ya Eid El-Adha kwa wahanga hao, akisihi suluhu ya kudumu ipatikane haraka.

Malalamiko makubwa yaliibuka dhidi ya mgambo waliotekeleza oparesheni hiyo, ambapo mwananchi Jane Francis Raphael, alijeruhiwa vibaya baada ya kusukumwa kwa nguvu na mgambo mmoja wakati akijaribu kuokoa mali zake zisiibwe.

Mbunge MwanaFA alihitimisha kwa kuwapoza wananchi na kuahidi kuwa atakuwa nao bega kwa bega hadi haki yao ya kikatiba na kisheria itakapopatikana nchini.




 

 


Na MWANDISHI WETU

TAASISI ya Saratani Ocean Road, imeungana na taasisi nyingine za afya katika banda la Wizara ya Afya katika viwanja vya Posta, Kijitonyama, kuangalia fainali ya UEFA Champion Leage.

Fainali hiyo ya UEFA inazikutanisha miamba ya soka barani Ulaya, Arsenal ya Ungereza na PSG ya nchini Ufaransa, ambapo mashabiki wengi wa Arsenali nchini Tanzania walijitokeza kwa wingi kuiunga mkono timu yao.

Mashabiki hao wa Asernal walioudhuria katika viwanja hivyo walipata nafasi kupima afya zao katika banda la Taasisi ya Ocean Road pamoja na kupewa elimu kuhusu ugonjwa wa saratani.

Katika shangwe hizo mashabiki wengi walijitokeza kipima afya zao pamoja na kupata elimu kuhusu saratani mbalimbali kutoka Taasisi ya Saratani Ocean.

Wananchi wametakiwa kupima mara kwa mara kujua mwenendo wa afya zao, ikiwemo saratani mbalimbali, kwasababu saratani ukigundulika mapema ni rahusi kutibika.



KAMATI ya  Bunge ya kudumu ya Bajeti imeipongeza Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA)kwa kuanzisha kitengo maalumu kwa ajili ya walipakodi wakubwa hatua ambayo imechangia ongezeko la kodi inayokusanywa na mamlaka hiyo.

Aidha Kamati hiyo imewatoa hofu wananchi juu ya dhana ya uwepo wa upendeleo wa kutolipa kodi kwa walipa kodi wakubwa ikisisitiza kuwa kila mwenye wajibu wa kulipa kodi kwa Mamlaka hiyo analipa kulingana na kiwango kile kile anachostahili.

Akizungumza wakati wa ziara ya kamati hiyo kutembelea kitengo cha walipa kodi wakubwa Jijini Dar es Salaam Mei 30, 2026 Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mashimba Ndaki amesema kuboreshwa kwa mazingira  na kufanya kuwa kama 'faragha' kwa mlipa kodi mkubwa kumewavutia wengi na hivyo kufanya mapato kupaa.

"Kwa namna hali ilivyo, ni tofauti na miaka miwili iliyopita, Sasa hivi walipa kodi wakubwa wanachangia asilia 40 ya Kodi tunayoikusanya, hiki ni kiwango kikubwa ambacho msingi wake Mkuu ni kuboreshwa kwa mazingira kulikofanywa na TRA kwa hili tunawapongeza sana" amesema Mashimba.

Pamoja na hilo amesema TRA imepiga hatua kubwa kwa kuboresha huduma mbalimbali ikiwemo ya watumishi wake kuwa na lugha nzuri jambo linalowavutia wananchi wengi kulipa kodi kwa hiari tofauti na ilivyokuwa zamani ambapo Mamlaka hiyo ilikuwa ikiogopeka.

Kuhusu dhana ya upendeleo kwa walipa kodi wakubwa, Ndaki amesisitiza kuwa hilo siyo jambo la kweli na ndiyo maana walipa kodi hao wameweza kuchangia asilimia 40 ya kodi yote iliyokusanywa huku walipa kodi wengine wakichangia asilimia 60 zilizobaki.

Kwa upande wake Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Yusuph Juma Mwenda ameshukuru hatua ya Kamati ya Bunge kuzitembelea Mamlaka hiyo akidai kuwa ziara hiyo itazidi kuwahamasisha kuendelea kuboresha huduma zao.

Amesema TRA itaendelea kutenda haki kwa walipa kodi wote kwa kuzingatia madaraja yao  kwa yule anastahili kulipa kikubwa atalipa kikubwa, anayestahili kulipa kidogo atalipa kidogo na yule asiyestahili kulipa hatolipa kwa kuwa hiyo ndiyo utaratibu wa utendaji wa Mamlaka hiyo.

Amesema uwepo wa Ofisi hiyo kwa ajili ya walipa kodi wakubwa wakiwemo wenye makampuni mbalimbali zaidi ya 851 ambao wamechangia asilimia 40 sawa na Trilioni 14 ya kodi iliyokusanywa  Mwaka huu ni kielelezo tosha cha kuwa walipa kodi wakubwa wanalipa kodi.




 

▪️︎ Aagiza watumishi waliohusika na ubadhirifu wa zaidi ya shilingi milioni 500 Manyoni wakamatwe na fedha zirudishwe

▪️︎ Akemea rushwa, wizi wa fedha za umma na matumizi mabaya ya madaraka

▪️︎ Aonya viongozi wanaowaza vyeo badala ya kutatua changamoto za wananchi


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba ameagiza watumishi waliohusishwa na ubadhirifu wa zaidi ya shilingi milioni 500 katika Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni watafutwe popote walipo, wakamatwe na kuchukuliwa hatua za kisheria na kinidhamu huku fedha hizo zikirejeshwa serikalini.

"Wamechota fedha za wananchi. Watafutwe hata ambao walishahamishwa, popote walipo wakamatwe, wawekwe ndani na fedha za Serikali zirudi. Hii si fedha ya mtu binafsi, ni fedha ya wananchi," alisema Dkt. Mwigulu.

Dkt. Mwigulu ametoa agizo hilo leo Jumamosi Mei 30, 2026 alipozungumza na wananchi wa Wilaya ya Manyoni katika Viwanja vya Tambukareli mkoani Singida akiwa katika ziara ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo, kusikiliza na kutatua changamoto za wananchi.

Alisema taarifa alizopokea zinaonesha kuwa jumla ya zaidi ya shilingi milioni 501 zilichotwa kutoka akaunti mbalimbali za halmashauri ikiwemo Akaunti ya Maendeleo (zaidi ya shilingi milioni 213), Akaunti ya Amana (zaidi ya shilingi milioni 259) na Akaunti ya Mapato ya Ndani (zaidi ya shilingi milioni 42), jambo ambalo haliwezi kuvumiliwa na Serikali.

Waziri Mkuu aliwataja watumishi wanaodaiwa kuhusika katika ubadhirifu huo kuwa ni aliyekuwa Mweka Hazina wa Halmashauri hiyo Mwakapala, ambaye kwa sasa amehamishiwa mkoani Songwe, Mhasibu wa Mapato Edward Kilungu na Eliamini Maliki.

Aidha, alimwagiza Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida (RPC) kuhakikisha watumishi hao wanatafutwa, wanakamatwa na kuwekwa mahabusu hadi fedha za Serikali zitakapopatikana.

"Mweka Hazina Mwakapala arudishwe, Edward Kilungu na Eliamini Maliki watafutwe. Wakamatwe, wawekwe ndani na wasitoke mpaka fedha ya Serikali irudi," alisema Dkt. Mwigulu.

Aidha, Waziri Mkuu alimuagiza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI kuhakikisha watumishi wote waliohusika wanasimamishwa kazi mara moja huku taratibu za kinidhamu na kisheria zikiendelea.

"Barua za kuwasimamisha kazi zitoke leo leo na hatua zinazostahili za kiutumishi zifanyike haraka. Wasitoke mpaka fedha za wananchi zirudi," alisema.

Sambamba na hilo, Dkt. Mwigulu alikemea vitendo vya rushwa, ubadhirifu wa mali za umma na matumizi mabaya ya madaraka, akieleza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita haitamvumilia mtu yeyote atakayehujumu rasilimali za wananchi.

"Ninachukia uvivu, uzembe, wizi na kuonewa kwa wanyonge. Nitawashikisha adabu wezi, walaghai na wote wanaotumia nafasi zao kuwaumiza wananchi," alisema.

Aidha, alimpongeza Mkuu wa Mkoa wa Singida pamoja na vyombo vya Serikali kwa kugundua na kuanza kuchukua hatua dhidi ya ubadhirifu huo.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu alikemea tabia ya baadhi ya viongozi kutumia muda mwingi kufikiria uchaguzi na vyeo badala ya kutatua changamoto za wananchi, akisisitiza kuwa Watanzania wanahitaji maendeleo na huduma bora zaidi kuliko siasa za makundi.

"Watanzania wana kiu ya maendeleo. Kiu waliyonayo si ya kugawana madaraka, bali ni maendeleo na kuondoka kwa kero zinazowakabili katika maisha yao ya kila siku," alisema.

Aliongeza kuwa viongozi wanapaswa kutumia nafasi walizopewa kutatua matatizo ya wananchi badala ya kutumia muda mwingi kufuatilia nafasi nyingine za uongozi.

"Kila mmoja afanye kazi katika nafasi aliyopewa. Watanzania wana shida nyingi zinazohitaji ufumbuzi na si siasa za makundi au mbio za madaraka," alisema.

Pia, Waziri Mkuu alisema Serikali itaendelea kusimamia haki za wananchi, kuimarisha uwajibikaji katika utumishi wa umma na kuhakikisha fedha za maendeleo zinafika na kutumika kwa malengo yaliyokusudiwa.

Alisema Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kutekeleza hatua mbalimbali za kuboresha maisha ya wananchi ikiwemo kutoa elimu bila ada kwa Kidato cha Tano na Sita, Programu ya Samia Scholarship na kuondoa riba kwa mikopo ya elimu ya juu kwa wahitimu ambao hawajapata ajira.

Aidha, alieleza kuwa Serikali imeendelea kutekeleza miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo Mradi wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere, Reli ya Kisasa (SGR), miradi ya maji, afya, barabara na usambazaji wa umeme vijijini ili kuharakisha maendeleo na kuboresha huduma kwa wananchi.

Waziri Mkuu aliwahakikishia wananchi wa Manyoni na Watanzania kwa ujumla kuwa Serikali itaendelea kutatua changamoto zinazowakabili na kusimamia kikamilifu utekelezaji wa miradi ya maendeleo ili kuhakikisha matunda ya maendeleo yanawafikia wananchi wote.

"Niwahakikishie Watanzania kwamba yote yaliyomo kwenye Ilani na ahadi za Mheshimiwa Rais yataendelea kutekelezwa kwa manufaa ya wananchi," alisema.












- zaidi ya Sh milioni 126 zaokolewa katika kipindi cha miezi sita

- huduma za upatikanaji wa hewa tiba zaimarika katika hospitali ya mawenzi

- Zaidi ya Mitungi 3000 ya Oksijeni imezalishwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mawenzi katika kipindi cha miezi sita tangu mradi huo uanze kufanya kazi , hali iliyosaidia kuondoa changamoto ya upatikanaji wa hewa tiba katika hospitali hiyo.

Hayo yamebainishwa leo na Mganga Mfawidhi wa hospitali hiyo, Dk Abdillah Issah alipokuwa akisoma taarifa ya ya mradi huo mbele ya Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Kenani Kihongosi alipotembelea na kukagua mradi huo.

Akizungumza baada ya kusomewa taarifa ya mradi na kutembelea sehemu mbalimbali za mradi huo Kihongosi amesema mradi huo ni miongoni mwa uwekezaji mkubwa uliofanywa na serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa lengo la kuboresha huduma za afya kwa wananchi wa Kilimanjaro na maeneo jirani.

Kihongosi amesema kabla ya kusimikwa kwa mtambo huo hospitali ilikuwa ikikabiliwa na gharama kubwa za ununuzi na usafirishaji wa oksijeni kutoka nje ya mkoa, hali iliyokuwa ikiathiri ufanisi wa utoaji wa huduma.

“Kupitia uwekezaji huo, hospitali imefanikiwa kupunguza gharama za uendeshaji, kuimarisha huduma za wagonjwa mahututi na kuongeza uwezo wa kusambaza oksijeni katika vituo vingine vinavyohitaji huduma hiyo,” amesema kihongosi.

Katika hatua nyingine amewapongeza viongozi na watumishi wa hospitali hiyo kwa usimamizi mzuri wa huduma, akisisitiza mafanikio hayo yanaonesha namna serikali inavyoendelea kuboresha sekta ya afya na kusogeza huduma bora karibu na wananchi.

Awali akisoma taarifa ya mradi huo Dk Issah amesema mradi huo umegharimu jumla ya Sh bilioni 1.94 na katika kipindi cha miezi sita tangu mradi kuanza kufanya kazi mitungi 3,313 ya Oksijeni imezalishwa katika hospitali hiyo, hali iliyisaidia kuondoa changamoto ya upatikanaji wa hewa tiba.

Pia ameongeza kuwa hatua hiyo imesaidia hospitali hiyo kuokoa takribani Sh milioni 126 katika kipindi cha miezi sita baada ya kuanza kutumia mtambo wa kuzalisha hewa tiba ya oksijeni.

“Hatua hiyo imepunguza utegemezi wa ununuzi wa oksijeni kutoka kwa wazabuni wa nje na kuimarisha utoaji wa huduma za afya katika hospitali ya Mawenzi,” amesema Dk Issah.









Top News