Na Mwandishi Wetu

TANZANIA imeonyesha mafanikio makubwa katika kupanua upatikanaji wa nishati safi ya kupikia, ambapo kiwango cha kitaifa cha upatikanaji kimeongezeka kutoka asilimia 6.9 mwaka 2021 hadi asilimia 28.6 mwaka 2025.

Ongezeko hilo la mara nne zaidi, linadhihirisha athari za jitihada mahsusi za serikali, dhamira ya kisiasa na ushirikiano na wadau wa maendeleo pamoja na sekta binafsi.

Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, kutoka Wizara ya Nishati, Mhandisi Innocent Luoga, ameyasema hayo jijini Dar es Salaam wakati wa Maadhimisho ya Miaka 13 ya Mpango wa Energising Development (EnDev) nchini.

Amesema mafanikio hayo yanaonyesha dhamira ya Tanzania kuhakikisha wananchi wanapata nishati safi, salama na nafuu ya kupikia na kwamba chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, kupikia safi kumepewa kipaumbele cha kitaifa na kuingizwa katika Dira ya Maendeleo ya Taifa ya Mwaka 2050.

Mhandisi Luoga ameeleza kuwa, Mkakati wa Kitaifa wa Kupikia Safi 2024–2034 unalenga kufikia asilimia 80 ya upatikanaji wa kupikia safi ifikapo mwaka 2034, huku National Energy Compact 2025–2030 ikilenga asilimia 75 ifikapo mwaka 2030.

Ameongeza ingawa kumekuwa na mafanikio, zaidi ya asilimia 70 ya Watanzania bado wanategemea kuni na mkaa, hali inayochangia uchafuzi wa hewa majumbani, uharibifu wa mazingira na mzigo wa muda kwa wanawake na watoto.

Kupitia mpango wa EnDev, changamoto hizo zimepunguzwa kwa kusambaza teknolojia nafuu na bora za kupikia, hususan Jiko Matawi linalozalishwa nchini.

Majiko hayo hupunguza matumizi ya kuni kwa hadi asilimia 40, kuboresha ustawi wa kaya na kusaidia uhifadhi wa misitu pamoja na juhudi za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Tangu mwaka 2013 hadi 2026, EnDev imefanikisha upatikanaji wa suluhisho za taa za sola kwa takribani watu 300,000 na suluhisho za kupikia safi kwa watu milioni 2 kupitia majiko bora na teknolojia za kupikia kwa umeme.

Mpango huo umewezesha zaidi ya wazalishaji 120 wa Jiko Matawi kufanya kazi katika mikoa 20, na hivyo kuunda ajira na kuimarisha ujasiriamali wa ndani.

Aidha, Mhandisi Luoga amesifu kuanzishwa kwa Chama cha Kitaifa cha Wazalishaji wa Jiko Matawi, akisisitiza kuwa serikali itaendelea kuunda mazingira wezeshi kupitia mageuzi ya sera, uendelezaji wa masoko na upatikanaji wa fedha. Amesema mafanikio ya EnDev yanatoa msingi thabiti wa kupanua suluhisho za nishati safi na kuboresha maisha ya mamilioni ya kaya nchini.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa SNV Tanzania, Mary Rauscher, amesema kwa zaidi ya muongo mmoja, EnDev imepanua upatikanaji wa nishati safi, nafuu na endelevu kwa karibu watu milioni 2, hususan vijijini na maeneo yaliyokuwa hayajahudumiwa.

Ameongeza kuwa kupitia mbinu za soko, mpango huu umechochea ukuaji wa sekta binafsi, kuwawezesha wajasiriamali wa ndani na kuimarisha mnyororo mzima wa thamani kuanzia kupikia safi hadi suluhisho za solar off-grid.

Rauscher amesisitiza kuwa maendeleo endelevu yanahitaji mageuzi ya mifumo katika sekta za nishati, kilimo na maji.SNV inalenga kuimarisha taasisi, kuwezesha masoko jumuishi na kushughulikia mizizi ya ukosefu wa usawa.

Amesisitiza kuwa usawa wa kijinsia na ujumuishaji wa kijamii ni kiini cha kazi zao, kuhakikisha wanawake, vijana na makundi yaliyotengwa si wadau pekee bali pia ni wahamasishaji wakuu wa mabadiliko.










Na Said Mwishehe,Michuzi TV

BENKI ya NMB imezindua rasmi NMB Mkononi Super App ikiwa ni jukwaa jipya la kidijitali linalolenga kubadili namna Watanzania wanavyosimamia maisha yao ya kifedha kwa kuweka huduma mbalimbali za benki, uwekezaji, akiba, mikopo na bima katika mfumo mmoja wa kisasa.

Akizungumza leo Juni 16,2026 jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi huo, Mkurugenzi Mkuu na Ofisa Mtendaji Mkuu wa NMB, Ruth Zaipuna amesema uzinduzi wa Super App hiyo unaashiria mwanzo wa enzi mpya ya huduma za kifedha nchini zinazokidhi mahitaji ya kizazi cha sasa na cha baadaye.

"Kuzingatia mahitaji ya leo na ya kesho, tunapoizindua Super App tunazindua namna mpya ya Watanzania kusimamia maisha yao ya kifedha, namna mpya ya kulinda maisha yao kupitia bima, namna mpya ya kuwekeza na kuweka akiba," amesema.

Amesema dunia imebadilika kwa kasi ambapo huduma nyingi sasa zinapatikana kupitia simu za mkononi, hivyo ni muhimu sekta ya fedha nayo kwenda sambamba na mabadiliko hayo.

"Leo watu wanasoma kupitia simu, wanasafiri kupitia simu, wanawasiliana kupitia simu na hata maisha yao ya kila siku yako kwenye simu. Sasa tumekusanya huduma zote muhimu za kifedha sehemu moja kwa urahisi, usalama na kasi inayoendana na mahitaji ya mteja wa sasa," amesema.

Zaipuna amesema NMB imeboresha mfumo huo baada ya kusikiliza maoni ya wateja wake waliotaka huduma nyingi zaidi zipatikane kupitia programu moja.

Miongoni mwa maboresho hayo ni uwezo wa mteja kuona akaunti zake zote katika sehemu moja bila kulazimika kutumia mifumo tofauti, pamoja na uwezo wa kuziunganisha mwenyewe ndani ya programu.

Aidha, amesema wateja sasa wanaweza kuweka standing orders kupitia simu zao, jambo litakalowarahisishia kufanya uhamisho wa fedha au kuweka akiba kwa wakati bila kukumbushwa kila mwezi.

Kwa mujibu wa Zaipuna, Super App hiyo pia imeongeza uwezo wa kufungua akaunti mpya kidijitali bila kufika tawi lolote la benki.

"Mteja hatahitaji kufika benki wala tawi lolote. Ataweza kufungua akaunti yake mwenyewe kupitia simu yake popote alipo," alisema.

Aliongeza kuwa mfumo huo unamwezesha mteja kupata taarifa mbalimbali za kifedha, kufuatilia mwenendo wa matumizi na kufanya maamuzi bora ya kifedha kupitia taarifa zinazopatikana ndani ya programu.

Zaipuna alisema hata watu ambao si wateja wa NMB sasa wanaweza kupakua programu hiyo na kuanza safari ya kujiunga na huduma za benki kwa urahisi.

Kuhusu huduma za mikopo, alisema kupitia Super App mteja binafsi anaweza kuomba mkopo wa hadi shilingi milioni mbili moja kwa moja kupitia simu yake, huku wafanyabiashara wadogo na wa kati wakipata fursa ya kuomba mikopo ya hadi shilingi milioni tano.

Amesema mafanikio hayo yametokana na uwekezaji mkubwa wa teknolojia uliofanywa na benki hiyo katika kipindi cha miaka mitano iliyopita ili kuhakikisha huduma zake zinakidhi viwango vya kimataifa.

Katika kuelezea umuhimu wa programu hiyo kwa vijana, Zaipuna alisema kizazi cha sasa kinahitaji huduma zinazopatikana muda wote na zinazokwenda sambamba na kasi ya maisha ya kidijitali.

"Vijana wa leo wanataka kusimamia fedha zao kupitia simu. Simu imekuwa biashara, benki na sehemu ya maisha yao ya kila siku. Hii Super App imejengwa kwa ajili yao na kwa ajili ya Watanzania wote," amesema.

Amewahimiza pia wabunifu wa teknolojia na wajasiriamali wa kidijitali kutumia fursa iliyopo ndani ya mfumo huo kuendeleza ubunifu wao kwa kushirikiana na NMB.

Kwa mujibu wake, benki hiyo inayohudumia zaidi ya wateja milioni 10 inalenga kuifanya Super App kuwa jukwaa la huduma mbalimbali za kifedha na biashara.

Zaipuna amesema moja ya huduma muhimu zilizoboreshwa ni usimamizi wa vikundi vya kijamii na kiuchumi kupitia mfumo huo.

Amesema vikundi vitaweza kufungua akaunti, kuwaalika wanachama, kuweka kanuni zao za uendeshaji, kusimamia michango, mikopo ya ndani na kutoa taarifa za kifedha kwa uwazi zaidi bila kulazimika kukutana ana kwa ana.

"Vikundi vimekuwa shule ya kwanza ya elimu ya fedha kwa Watanzania wengi. Kupitia mfumo huu vitapata uwazi, usalama na ufanisi zaidi katika usimamizi wa fedha zao," amesema.

Ameeleza kuwa wanachama wataweza kuona michango yao, taarifa za kifedha na kushiriki maamuzi muhimu popote walipo kupitia simu zao.

Katika hatua nyingine, amesema Super App hiyo imeanza pia kutoa huduma za ununuzi wa bima kidijitali, ikiwemo bima za magari, pikipiki na mali dhidi ya moto.

Kwa mujibu wake, mteja anaweza kujinunulia bima au kumnunulia mtu mwingine kwa kutumia taarifa za msingi kama namba ya usajili wa gari au taarifa nyingine zinazohitajika, hatua inayorahisisha upatikanaji wa huduma za bima nchini.

Amesisitiza uzinduzi wa NMB Mkononi Super App ni sehemu ya mkakati wa benki hiyo kuendelea kuongoza mapinduzi ya huduma za kifedha kidijitali nchini kwa kuwapatia Watanzania huduma salama, rahisi na zenye kasi zinazowawezesha kufikia malengo yao ya kifedha.






Katika jamii ya Kimaasai, maisha ya mwanaume hupitia hatua mbalimbali za kimila zinazoonyesha ukuaji, Miongoni mwa hatua hizo muhimu ni kufanyiwa sherehe inayojulikana kwa jina la Orkiteng le Sirit ikimaanisha ni mwisho wa ujana na kuingia uzeeni.

Katika hatua hii ambapo mtu anatawazwa kuingia rika la uzee, wazee wa jamii hiyo huchagua Dume la rika ambalo lina afya njema na lililohasiwa tangu utoto wake, dume hili siku ya shughuli ndio hutolewa mwanzo kwenye boma lenye  Ng’ombe wengi na kumwagiwa maziwa kisha hunyongwa hadi kufa. 

Sherehe ya Orkiteng le Sirit , si sherehe ya kawaida bali ni tukio la heshima kubwa linalofanyika kwa kufuata mila na desturi za kale zilizorithishwa kutoka kizazi hadi kizazi. Kwa jamii ya Kimaasai, ni hatua ya ukamilifu wa mwanaume na uthibitisho kwamba ametimiza majukumu yake ya kifamilia na kijamii, kufanyiwa sherehe hii hakuangalii umri ila inazingatia jinsia kwa kuwa anayefanyiwa sherehe hii ni mwanaume pekee, vigezo vinavyoangaliwa ili mwanaume afanyiwe sherehe hii, ni lazima awe ameoa, awe na watoto wa kike na kiume na awe mtu mwema na maadili katika jamii.

Akizungumza wakati wa sherehe hiyo, Alaigwanani wa kabila la kimasai Maningo Rinjo amesema viongozi wa mila wa ukoo kama (Laizer, Mollel, Laitayo, Ngidong’i) ndio wenye jukumu la kumchagua dume atakayechinjwa baada ya kujiridhisha kuwa ana sifa zote zinazotakiwa kwa mujibu wa mila na desturi za Kimaasai ili kutekeleza jukumu hilo la kijamii ambalo linahudhuriwa na ndugu wote wa familia na jamii yote ya wamasai inayozunguka Kijiji hicho. 

“Si kila dume anaruhusiwa kutumika katika sherehe hii, sisi viongozi wa mila hukagua na kuthibitisha sifa zake kabla ya kutoa ruhusa ya kuchinjwa, dume wa kutekeleza sherehe hii lazima awe amehasiwa tangu utotoni, hajawahi kumpanda dume jike, pembe zake ziwe zimenyooka bila kupinda mithili ya pembe za mbogo, asiwe mgonjwa na sifa zingine za ndani ambazo viongozi wa kimila ndio huzichunguza kwa undani,” alisema Alaigwanani Maningo Rinjo.

Alaigwanani Olonyori Lemoyan kutoka Ukoo wa Laizer Kata ya Nainokanoka Ngorongoro alisisitiza kuwa si kila mwanaume anastahili kufanya sherehe ya Orkiteng le Sirit, moja wa masharti muhimu ili mwanaume afanyiwe tukio hilo kuwa

na familia yenye watoto wa kike na kiume, awe na mali na uelekeo wa maisha, mtu anayejali watu na awe ni rafiki wa ukoo wake na jamii inayomzunguka pamoja na kupata ridhaa ya ukoo wake kufanya sherehe hiyo. 

“Orkiteng le Sirit ni heshima kubwa katika jamii ya Kimaasai. Mwanaume lazima awe ametimiza wajibu wake wa kifamilia kwa kupata watoto wa kike na wa kiume. Bila kutimiza sharti hilo, hawezi kufikia hatua hii muhimu ya maisha,” alisema Alaigwanani Olonyori Lemoyan.

Wakati wa sherehe hizo baada ya dume kunyongwa na kutolewa nyama zake, mwanaume anayehitimu (anayepandishwa rika) pamoja na mke wake na mama yake mzazi wanatakiwa hukalia utumbo wa dume hilo kama ishara ya kuaga rasmi ujana na kuingia katika hatua ya uzee. Kitendo hicho hubeba maana kubwa ya kiutamaduni na kuashiria mwanzo wa jukumu jipya ndani ya jamii na kuachana na usharobaro na mambo yote ya ujana.

Baada ya taratibu hizo kukamilika, rika la Korianga huungana na mwenzao aliyeingia hatua ya uzee timilifu huimba nyimbo za furaha na heshima huku wakielekea bomani, wakimpongeza mwenzao kwa kufikia hatua hiyo adhimu. Nyimbo hizo huashiria kukubalika kwake rasmi katika kundi la wazee na kupewa nafasi ya kushiriki kikamilifu katika mila, desturi na maamuzi yanayohusu ustawi wa jamii.

Orkiteng le Sirit si tu sherehe ya kuchinja dume laa hasha, ni alama ya mafanikio ya maisha, uwajibikaji wa kifamilia na heshima ya kuwa mzee katika jamii ya Kimaasai. Hatua hii ni urithi wa kipekee unaoendelea kuunganisha vizazi na kuhifadhi utamaduni wenye thamani kubwa kwa jamii hiyo.













Na GULATONE MASIGA


Katika zama za teknolojia na mawasiliano ya kidijitali, mitandao ya kijamii imekuwa sehemu muhimu ya maisha yetu ya kila siku. Kupitia majukwaa mbalimbali, wananchi wanapata habari, wanabadilishana mawazo, wanafanya biashara, wanajifunza na hata kushiriki katika mijadala ya masuala ya kitaifa na kimataifa.

Hata hivyo, pamoja na manufaa hayo makubwa, mitandao ya kijamii imegeuka kuwa chombo kinachoweza kutumika vibaya kueneza chuki, taarifa za uongo, uchochezi na hamasa zinazoweza kuhatarisha amani na utulivu wa jamii.

Kwa siku za karibuni, Tanzania imeshuhudia kampeni na hamasa kubwa katika baadhi ya mitandao ya kijamii zinazohamasisha vurugu, ghasia na uvunjifu wa sheria kwa madai ya kudai haki au kuonyesha kutoridhika na hali fulani za kisiasa na kijamii.

Wakati haki ya kutoa maoni ni msingi muhimu wa demokrasia, ni lazima kutofautisha kati ya maoni yenye kujenga na uchochezi unaoweza kusababisha madhara kwa taifa zima.


Somo Kutoka Kumbukumbu za Oktoba 2025


Watanzania wengi bado wanakumbuka yaliyotokea mwezi Oktoba 2025. Kilichoanza kama kampeni na hamasa katika mitandao ya kijamii kiligeuka kuwa hali iliyosababisha taharuki, hofu na maumivu kwa sehemu mbalimbali za nchi.

Kulishuhudiwa matukio ya vifo na majeruhi. Miundombinu ya umma iliharibiwa na kuchomwa moto. Baadhi ya biashara na mali binafsi ziliporwa au kuharibiwa. Usafiri ulitatizika katika maeneo mbalimbali, huku wananchi wa kawaida wakibeba mzigo mkubwa wa madhara yaliyotokana na yaliyoitwa maandamano ya amani.

Athari zake hazikuishia kwa waliohusika moja kwa moja pekee. Wafanyabiashara walipoteza mitaji yao. Wanafunzi walikosa utulivu wa kujifunza. Wawekezaji walipata wasiwasi kuhusu mazingira ya biashara. Familia nyingi ziliishi katika hofu na sintofahamu.


Haya ni maumivu ambayo hayapaswi kusahaulika kwa urahisi.


Ukweli Mchungu wa Mitandao ya Kijamii


Moja ya mambo yanayopaswa kutafakariwa kwa kina ni kwamba sehemu kubwa ya wanaohamasisha vurugu na machafuko hawapo maeneo ambayo matukio hayo yanatokea. Wengine wako maelfu ya kilomita mbali katika nchi za Ulaya, Marekani au maeneo mengine duniani.

Wao hawatakutana na moshi wa matairi yanayowaka. Hawatapoteza biashara zao. Hawatakuwa kwenye foleni za dharura hospitalini. Hawatapoteza ajira wala kuhangaika na usafiri au kutafuta chakula kwa sababu shughuli za kiuchumi zimesimama.

Mara nyingi, anayepata madhara ni mwananchi wa kawaida. Ni mama lishe anayekosa wateja. Ni dereva anayekosa safari. Ni mfanyabiashara anayepoteza mtaji wake. Ni mwanafunzi anayekosa masomo. Ni taifa lote linalopoteza muda na rasilimali ambazo zingeelekezwa katika maendeleo mengine zinatumika kujenga upya miundombinu iliyoharibiwa na kuhudumia waathirika.

Ndiyo maana ni muhimu kila Mtanzania kutambua kuwa si kila ujumbe unaosambaa mtandaoni unapaswa kufuatwa bila kuhoji. Elimu ya kidijitali inahitaji uwezo wa kuchambua taarifa, kutambua propaganda, na kupima matokeo ya kile kinachohamasishwa.


Amani ni Mtaji wa Maendeleo


Tanzania imejijengea sifa ya kuwa taifa la amani, umoja na mshikamano kwa miongo mingi. Hii si bahati mbaya. Ni matokeo ya juhudi za viongozi, taasisi na wananchi waliotanguliza maslahi ya taifa mbele ya tofauti zao.

Amani ndiyo imewezesha uwekezaji katika sekta mbalimbali. Ndiyo imewezesha ujenzi wa shule, hospitali, barabara, miradi ya maji na umeme. Ndiyo imewezesha biashara kukua na vijana kupata fursa za ajira.

Historia inaonesha kuwa pale ambapo amani inapotoweka, maendeleo husimama. Wawekezaji huondoka. Uchumi hudorora. Huduma za kijamii huathirika. Mwisho wa siku, gharama hulipwa na wananchi wenyewe.

Kwa sababu hiyo, amani si jambo la kuchukuliwa kawaida. Ni rasilimali ya taifa inayohitaji kulindwa kila siku.


Matumizi Chanya ya Mitandao ya Kijamii


Badala ya kutumia mitandao ya kijamii kueneza chuki, vurugu au taharuki, kuna fursa kubwa zaidi za kuitumia kwa manufaa ya jamii.

Vijana wanaweza kuitumia kujifunza ujuzi mpya, kutangaza biashara zao, kutafuta masoko, kuhamasisha shughuli za maendeleo na kujenga mitandao ya kitaaluma.

Wananchi wanaweza kuitumia kutoa maoni kwa staha, kuibua changamoto za jamii na kushiriki katika mijadala yenye kujenga suluhisho.

Mitandao ya kijamii inaweza kuwa daraja la maendeleo au chanzo cha migogoro. Mwelekeo wake unategemea namna tunavyoichagua kuitumia.


Wajibu wa Kila Mtanzania


Katika kipindi hiki ambacho taarifa husambaa kwa kasi kubwa, kila Mtanzania ana wajibu wa kuwa mlinzi wa amani.

Tusisambaze taarifa ambazo hatujazithibitisha. Tusikubali kutumiwa kama vyombo vya kueneza chuki au uchochezi. Tujiulize kila mara: Je, ujumbe ninaoshiriki kuusambaza unajenga au unabomoa? Unaleta suluhisho au unachochea mgogoro?

Tofauti za maoni ni sehemu ya jamii yoyote ya kidemokrasia. Lakini tofauti hizo zinapaswa kushughulikiwa kwa njia za kistaarabu, za kisheria na zinazolinda maisha na mali za wananchi.


Hitimisho

Watanzania walipata somo kubwa kutokana na matukio ya Oktoba 2025. Somo hilo linapaswa kutukumbusha kuwa amani ikivurugika, hakuna anayebaki salama. Madhara yake huwagusa wote bila kujali itikadi, dini, kabila au hali ya kiuchumi.

Tusikubali tena kuingia katika mkumbo wa hamasa zinazoweza kusababisha machafuko, vurugu na uharibifu. Badala yake, tuutumie uwezo wa teknolojia na mitandao ya kijamii kujenga uchumi, kuimarisha umoja wa kitaifa, kuitangaza Nchi yetu kwa uzuri wake na kuharakisha maendeleo ya nchi yetu.

Amani ya Tanzania ni wajibu wa kila Mtanzania. Tukiilinda leo, tutakuwa tumelinda ustawi wa kizazi cha sasa na vizazi vijavyo.


Kwa Maoni Na Ushauri

0768497974


Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Wabunge wameipongeza Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) kwa kuendelea kupanua wigo wa huduma za hifadhi ya jamii kupitia Skimu ya Hifadhi kwa Wananchi Waliojiajiri, wakisema mpango huo unatoa fursa kwa mamilioni ya Watanzania kunufaika na huduma za hifadhi ya jamii.

Aidha, wamepongeza uwekezaji uliofanywa na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) katika Kiwanda cha Kimataifa cha Bidhaa za Ngozi cha Kilimanjaro (KLICL), wakisema mradi huo una mchango mkubwa katika kukuza viwanda, kuongeza thamani ya mazao ya mifugo na kutengeneza ajira.

Pongezi hizo zilitolewa Juni 15, 2026 jijini Dodoma wakati wa semina ya wabunge kuhusu Skimu ya Hifadhi kwa Wananchi Waliojiajiri na Mradi wa Kiwanda cha Kimataifa cha Bidhaa za Ngozi cha Kilimanjaro.

Akizungumza kwa niaba ya Spika wa Bunge, Mhe. Mussa Azzan Zungu, Naibu Spika wa Bunge, Mhe. Daniel Sillo, aliipongeza NSSF pamoja na PSSSF kwa kuendelea kutoa elimu kwa wabunge kuhusu masuala ya hifadhi ya jamii na miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa na mifuko hiyo.

Mhe. Sillo alisema elimu hiyo ni muhimu kwa wabunge kwani itawawezesha kuwa mabalozi wa kuhamasisha wananchi katika majimbo yao kujiunga na mifumo ya hifadhi ya jamii na kufahamu uwekezaji unaofanywa na mifuko hiyo.

Baadhi ya wabunge walioshiriki semina hiyo, akiwemo Mhe. Said Salimu na Mhe. Rashid Shangazi, waliipongeza NSSF kwa juhudi zake za kuwafikia wananchi waliojiajiri na kuimarisha huduma za hifadhi ya jamii nchini.

Walisema skimu hiyo itasaidia kujenga utamaduni wa kuweka akiba, kuongeza usalama wa kipato na kuwapa wananchi waliojiajiri fursa ya kunufaika na huduma za hifadhi ya jamii.

Kwa upande wa uwekezaji wa PSSSF, wabunge Jackson Kiswaga na Rashid Shangazi waliipongeza PSSSF kwa uwekezaji kwenye kiwanda hicho, huku wakiishauri sekta binafsi ikaribushwe katika uendeshaji wa kiwanda ili kuongeza nguvu katika masoko na uzalishaji.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu, alisema Serikali inaendelea kuimarisha huduma za hifadhi ya jamii kwa kuwajumuisha wananchi waliojiajiri, ambao kwa muda mrefu walikuwa nje ya mifumo rasmi ya hifadhi ya jamii licha ya mchango wao mkubwa katika uchumi wa taifa.

Kuhusu PSSSF, Mhe. Sangu alisema mradi wa kiwanda hicho unamilikiwa kwa ubia kati ya Mfuko huo na Jeshi la Magereza kupitia kampuni yake ya Prisons Corporation Sole (PCS) na kuwa umekuwa na manufaa makubwa kwa jamii na taifa kwa ujumla.

Awali, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Bw. Masha Mshomba, alisema mfuko huo unalenga kuandikisha wananchi waliojiajiri milioni 3.7 ifikapo Juni 2031 kupitia Skimu ya Hifadhi ya Jamii. Alisema takribani asilimia 85 ya nguvu kazi nchini, sawa na wananchi milioni 20.98 wenye uwezo wa kufanya kazi, wamejiajiri, jambo linaloifanya skimu hiyo kuwa nyenzo muhimu ya kuwafikia makundi mbalimbali ya wananchi.

Bw. Mshomba alisema wanachama wa skimu hiyo watanufaika na mafao mbalimbali yakiwemo pensheni ya uzee, mafao ya urithi, ulemavu, uzazi na matibabu. Alisema wananchi sasa wanaweza kujiunga, kuchangia na kufuatilia taarifa zao kwa njia za kidijitali kupitia simu za mkononi, huku kiwango cha chini cha mchango kikiwa shilingi 30,000 kwa mwezi.

Naye, Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF, Bw. Fortunatus Magambo, amesema kiwanda hicho kinazalisha bidhaa zenye ubora wa hali ya juu na kimekuwa na mchango mkubwa kwa jamii na taifa kwa ujumla.

Alisema kiwanda hicho kimeongeza ajira kwa wananchi, kimeboresha kipato cha wananchi hususan wafugaji kupitia upatikanaji wa soko la uhakika la ngozi, na kuchochea mnyororo wa thamani wa sekta ya mifugo nchini.

“Kiwanda chetu kinazalisha bidhaa zenye ubora mkubwa, kimeongeza ajira kwa wananchi na kimefungua soko la uhakika la ngozi kwa wafugaji wetu, jambo linalonufaisha jamii na taifa kwa ujumla,” alisema Bw. Magambo.

























-Atoa maagizo lukuki ya kuboresha Mkoa huo kuelekea AFCON 2027.


-Ataka muonekano mzuri wa Jiji kwa kufanya usafi wa mazingira na kuondoa kabisa gereji bubu barabarani.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Albert Chalamila ametoa muda wa mwezi mmoja kwa wamiliki wa gereji na mafundi seremala kuondoa vyuma chakavu na samani chakavu maeneo ya barabarani ili jiji liwe nadhifu huku akiwataka Madiwani, wenyeviti wa mitaa,watendaji wa kata na mitaa pamoja na wakuu wa wilaya zote tano kushiriki kikamilifu katika ulinzi na usalama wa maeneo yao na Mkoa huo kwa ujumla ikiwemo kuanzisha vikundi vya sungusungu

Akizungumza katika katika kikao kazi maalum kilichokutanisha Madiwani, wenyeviti wa mitaa,watendaji wa Kata na Mitaa pamoja na wakuu wa wilaya zote tano za Mkoa huo Mkuu wa Mkoa Albert Chalamila amesema vyuma hivyo chakavu kwenye maeneo ya barabara vimekuwa vikiharibu muonekano wa jiji huku pia akisisitiza serikali mkoani humo haitokuwa tayari kuona amani ya mkoa huo inavurugwa kwa kuwa mkoa huo ndio kitovu cha masuala ya kidiplomasia na uchumi

Aidha amezungumzia taarifa zinazosambaa mitandaoni juu ya uwepo wa watu wanaofikiria kufanya maandamano ambapo amewataka viongozi na mitaa na kata kuendelea kusimamia amani kwenye mitaa na kata zao

Sanjari na hayo Mkuu wa Mkoa Mhe Albert Chalamila amewataka viongozi wa wangazi za mitaa na kata kuimarisha usafi wa mazingira ili kuepukana na maradhi ya mlipuko na watambue kuwa Tanzania imepata fursa ya kuwa mwenyeji wa mashindano ya AFCON,hivyo haitokuwa vyema kuona heshima hiyo ambayo Taifa imepata inaharibiwa kutokana na uzembe kwenye suala la usafi na amewataka wakurugenzi kusimamia vyema sheria na kanuni za usafi wa mazingira ili kuimarisha usafi na kudhibiti tabia ya utupaji taka hovyo huku akisisitiza majengo ya barabarani kupaka rangi nyumba zao

Akizungumzia suala la mchakato wa uendeshaji wa dampo la pugu kinyamwezi kwa ubia na kampuni binafsi Chalamila ametoa muda wa hadi julai 30 kwa mchakato huo kuanza kwa mpango huo na amehimiza Halmashauri zote za jiji hilo kuwa na dampo la kutupia taka sanjari na kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kujua kutrndanisha taka na amepiga marufuku suala la ubandikaji wa picha za matangazo kwenue maeneo ya jiji hilo na amewstaka wakurugenzi kutotoa vibali vya bar kwenye makazi ya watu ikiwemo Masaki na Oystabay

Awali Katibu Tawala Mkoa wa Dar es salaam Ndg Abdul Mhinte amesisitiza suala la anuani za makazi kutumika vyema kutambua watu na makazi yao ili kusaidia kuimarisha Amani.







Na Janeth Raphael MichuziTv


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), chini ya uongozi wa Mwenyekiti wake Mhe. Devotha Minja, imekutana na uongozi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwa ajili ya kupokea, kupitia na kuchambua taarifa ya hesabu za taasisi hiyo kwa mwaka wa fedha unaoishia Juni 30, 2025, zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).

Katika kikao hicho, PAC imeielekeza TRA kuchukua hatua za haraka kurekebisha mapungufu yote yaliyoibuliwa na CAG, hususan katika maeneo ya ukusanyaji wa kodi na usimamizi wa mapato ya serikali.

Kamati hiyo pia imeitaka TRA kuimarisha mifumo yake ya usimamizi wa kodi kwa kuongeza ufanisi katika ukaguzi, uhakiki wa taarifa za walipakodi, pamoja na kuboresha mifumo ya ufuatiliaji wa mapato ili kuhakikisha hakuna upotevu wa fedha za umma.

Kwa upande wake, Kamishna Mkuu wa TRA, Yusuph Mwenda, amesema taasisi hiyo imepokea maelekezo yote ya PAC na kuyapa kipaumbele, huku akiahidi kuwa mapungufu yaliyobainishwa yatashughulikiwa ndani ya muda uliopangwa.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya TRA, Uledi Mussa, amesema kikao hicho kimekuwa fursa muhimu ya kujifunza na kubaini maeneo yanayohitaji kuimarishwa zaidi ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi na walipakodi.

Ameongeza kuwa lengo la TRA ni kuwa taasisi inayoaminika na wananchi, huku ikiendelea kuhamasisha ulipaji kodi kwa hiari kama njia ya kuongeza mapato ya ndani na kuchochea maendeleo ya taifa.

Pia ameiomba PAC kuendelea kuwa mabalozi wa kuelimisha na kuhamasisha wananchi kutimiza wajibu wao wa kulipa kodi kwa hiari ili kuunga mkono maendeleo ya nchi.








Na Oscar Assenga, Tanga

Mkoa wa Tanga unatarajia kuupokea Mwenge wa Uhuru Juni 17, mwaka huu, ambapo utakimbizwa katika halmashauri zote 11 za mkoa huo na kukagua, kuzindua pamoja na kuweka mawe ya msingi katika miradi 73 yenye thamani ya zaidi ya Sh bilioni 27.7.

Hayo yalisemwa leo na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dk. Batilda Burian, wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maandalizi ya mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2026.

Dk. Burian alisema Mwenge wa Uhuru utapokelewa katika Viwanja vya Shule ya Msingi Mji Mpya, Kijiji cha Mtoro, Kata ya Tunguli wilayani Kilindi ukitokea Mkoa wa Morogoro, kabla ya kukimbizwa kwa umbali wa kilometa 1,340 katika halmashauri zote za mkoa huo.

Alisema Juni 28, mwaka huu, Mwenge huo utakabidhiwa Mkoa wa Kilimanjaro katika Uwanja wa Shule ya Msingi Hedaru.

Kwa mujibu wa Mkuu huyo wa Mkoa, kati ya miradi 73 itakayofanyiwa kazi na Mwenge wa Uhuru, miradi 34 itawekewa mawe ya msingi, 26 itafunguliwa na kuzinduliwa, huku miradi 11 ya vijana na miradi miwili ya sekta ya maji ikikaguliwa.

Alifafanua kuwa miradi hiyo ina thamani ya Sh bilioni 27.76, ambapo Sh milioni 300.6 ni nguvu za wananchi, Sh bilioni 1.27 ni michango ya halmashauri, Sh bilioni 10.7 ni fedha za Serikali Kuu na Sh bilioni 15.47 ni kutoka kwa wahisani.

Akizungumzia kaulimbiu ya mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka huu inayosema, “Tanzania ni Yetu Sote, Tushikamane kwa Pamoja Kuleta Maendeleo,” Dk. Burian alisema mkoa umejipanga kuhakikisha wananchi wa makundi mbalimbali wanashiriki kikamilifu katika shughuli zote za Mwenge.

“Tumewaandaa viongozi wa serikali, watumishi wa umma, viongozi wa dini, wanawake, vijana, watu wenye mahitaji maalumu pamoja na makundi mengine kushiriki kikamilifu kuanzia mapokezi hadi makabidhiano ya Mwenge wa Uhuru,” alisema.

Aliongeza kuwa wananchi watapata fursa ya kuushika na kuukimbiza Mwenge huo kama sehemu ya kuimarisha mshikamano na umoja wa kitaifa unaosisitizwa katika kaulimbiu ya mwaka huu.

Mbali na kuhamasisha maendeleo, alisema Mwenge wa Uhuru utaendelea kutoa elimu kuhusu mapambano dhidi ya rushwa, malaria, VVU/UKIMWI, matumizi ya dawa za kulevya na umuhimu wa lishe bora.

Dk. Burian aliwataka wananchi wa Mkoa wa Tanga kujitokeza kwa wingi katika maeneo ya mapokezi, miradi na mikesha mbalimbali ili kushiriki shughuli za Mwenge wa Uhuru.

“Mkoa umejipanga kikamilifu kuhakikisha wananchi wanapata burudani na hamasa kupitia ushiriki wa wasanii na vikundi mbalimbali vya sanaa katika maeneo yote ambayo Mwenge wa Uhuru utakesha,” alisema.

Alisema kwa ujumla maandalizi ya kuupokea Mwenge wa Uhuru wa mwaka 2026 yamekamilika kwa kiwango cha kuridhisha na mkoa uko tayari kwa shughuli zote za mbio hizo.

Na.Ashura Mohamed - Arusha

Katika kuhakikisha kuwa Uchumi wa wakazi wa mkoa wa Arusha unaimarika wananchi wa mkoa huo hususani Vijana wametakiwa kuhakikisha kuwa wanachangamkia fursa mbali mbali za kiuchumi ili kunufaika na ujio wa mashindano ya kimataifa ya Afcon 2027.

Akizungumza kwa niaba ya mkuu wa Wilaya ya Arusha Mjini bw.Jospeh Mkude,wakati wa Kongamano la Vijana la Engutoto Youth Summit kuhusu Mashindano ya AFCON 2027,Wakili Irene Ndosi ambaye ni Katibu Tarafa Suye amesema kuwa ujio wa Afcon ni neema kubwa kwa wakazi wa mkoa wa Arusha ambapo mbali na kupata burudani ya mpira wa miguu lakini pia ni fursa kwa makundi yote kuongeza uchumi wao.

"Fursa zitaanzia kuanzia watu wa chini kabisa boda boda,watu wa usafirishaji mpaka wanawake watengeneza shanga,kila mtu achukue nafasi hiyo kuleta mabadiliko chanya kwenye uchumi wake binafsi na familia yake na mkoa kwa ujumla,pia tuwe tayari kujaza eneo la uwanja wa Afcon kwasababu mashindano haya ni yakipekee na yanashirika nchi tatu ambazo ni Tanzania,Kenya na Uganda."Amesitiza Ndosi

Aidha Hamza Juma Njiku ni Diwani wa Kata ya Engutoto amesema kuwa kongamano hilo ni muhimu kwa kuwa limewakutananisha vijana na wadau mbal8 mbali katika kuonyesha fursa zilizopo kuelekea mashindano hayo ya Afcon.

"Sisi katika kata yetu fursa za Afcon zimetugusa moja kwa moja kwa kuwa tunajengewa Uwanja mkubwa mzuri wa Mazoezi kwaajili ya mashindano hayo ambapo utakuwa na uwezo wa kuchukuwa watu 5000 waliokaa,maegesho ya magari 500 na mabasi mawili kwaajili ya zile timu ambazo zitaingia kufanya mazoezi,ila uwanja ukikamilika na mashindano kumalizika utatumika kwaajili ya ligi kuu na michuano mbali mbali."Amesema Diwani Njiku

Kwa Upande wake Mwenyekiti wa Umoja wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM),Kata ya Engutoto ambaye ndio muandaaji wa Kongamano Engutoto Youth Summit,bw.Ibzan Michael Ruheta amesema kuwa kongamano hili si jukwaa la kisiasa bali ni jukwaa linalokutanisha watu wote kujadili fursa za AFCON kuelekea mwaka 2027.

Bw.Ruheta amesema kuwa Mashindano ya AFCON hayatahuishwa na Tanzania peke yake bali ushirikiano na mataifa mengine wakiwemo Kenya pamoja na Uganda,hivyo kama Watanzania ni wajibu wao kuamka na kuhakikisha tunaitumia nafasi hiyo ipasavyo.

"Ndugu mgeni rasmi, kama unavyojua nchi yetu imepata fursa ya kuandaa mashindano haya ya AFCON,hivyo kama viongozi mliopo katika nafasi za maamuzi, ni vizuri kujipanga kwa kushirikiana na wadau mbalimbali na taasisi mbalimbali zilizopo nchi yetu kwa kikisha fursa hizi tunazipata kwa wakati, vijana waheshimiwe, wasikilizwe na kero zao zitatuliwe ili nchi yetu inufaike."Amefafanua Mwenyekiti huyo

Kongamano la Engutoto Youth Summit lenye kauli mbiu ya "Unlocking 2027 AFCON Opportunity" limeandaliwa na Vijana wa Chama Cha Mapinduzi Kata ya Engutoto,na limekusudia kuwajengea vijana uwezo wa kunufaika na fursa za michezo hiyo kubwa ya kimataifa ambapo limefanyika katika Chuo cha Uhasibu Arusha(IAA) na kukutanisha Vijana Zaidi ya 1000 ili kuonesha nyanja mbali mbali ambazo vijana wanaweza kunuifa nazo.
Picha ya Viongozi Mbali Mbali wa Chama na Serikali walioshiriki Kutoa Mada  katika Kongamano la Engutoto Youth Summit kupelekea Mashindano ya AFCON 2027.
Mgeni rasmi Wakili Irene Ndossi ambaye ni katibu Tarafa ya Suye akimwakilisha mkuu wa Wilaya ya Arusha Mjini akizungumza na Vijana ambao hawapo pichani
Mwenyekiti wa UVCCM Kata ya Engutoto mwenye Tisheti Nyeupe Bw.Ibzan Ruheta akiwa katika picha ya Pamoja na Wadau Mbali mbali
Safu ya Viongozi wa Chuo kutoka Chuo Cha Arusha Technical(ATC) ikiongizwa na Raisi wa Serikali ya wanafunzi  Bw.Magolosa Mosses mwenye  Suti nyeusi Kulia,mara baada ya kumalizika kwa Kongamano hilo katika Chuo Cha Uhasibu Arusha.


Top News