Na Mwandishi wetu, Mirerani 
MADINI ya Tanzanite ya thamani ya zaidi ya shilingi milioni 993 yameuzwa kwenye minada miwili iliyofanyika hivi karibuni katika jengo la Tanzanite Exchange Centre mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara.

Afisa madini mkazi Mirerani (RMO) George Kaseza, ameyasema hayo kwenye ziara ya Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo Kenani Laban Kihongosi alipotembelea jengo hilo na kukagua akiwa ameongozana na viongozi wa mkoa na wilaya.

Kaseza amesema minada miwili ilifanyika hivi karibuni ambapo mnada wa kwanza wa mabroka ulifanyika Mei 15 mwaka 2026 kwa washiriki 84 na madini ya shilingi 271,270,100 yalinunuliwa.

"Mnada wa pili wa dealers ulifanyika Mei 21 mwaka 2026 na madini ya thamani ya shilingi 721,750,000 yalinunuliwa," amesema RMO Kaseza.

Amesema jengo la Tanzanite Exchange Centre linamilikiwa na Halamshauri ya Wilaya ya Simanjiro ila linaendeshwa na Tume ya Madini kupitia ofisi yake.

Katibu wa NEC, Itikadi Uenezi na Mafunzo Kenani Laban Kilongosi amewapongeza watumishi wa ofisi ya RMO Mirerani kwa namna wanavyofanya kazi katika eneo hilo.

Kenani amesema tayari soko hilo limeanza kuonyesha matokeo chanya ya uwekezaji huo kutokana na mwitikio mkubwa wa wafanyabiashara na mafanikio ya minada iliyofanyika ndani ya muda mfupi tangu kuanza kutumika.





WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amehitimisha ziara yake ya kikazi mkoani Iringa kwa kuwataka viongozi na watumishi wa umma kuendelea kusimamia haki, uwajibikaji na utoaji wa huduma bora kwa wananchi pamoja na kufuatilia utekelezaji wa maelekezo yote yaliyotolewa katika kutatua kero za wananchi.

Ametoa maelekezo hayo leo Jumapili (Juni 7, 2026) wakati akifunga ziara yake ya kikazi mkoani Iringa kwa kufanya kikao cha majumuisho na viongozi pamoja na watumishi wa umma kilichofanyika katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa.

Dkt. Mwigulu amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imewekeza fedha nyingi katika sekta mbalimbali za maendeleo hivyo ni wajibu wa viongozi na watumishi kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na haki zao zinalindwa.

Amesema ameridhishwa na namna Mkoa wa Iringa ulivyoshughulikia changamoto mbalimbali za wananchi na kuwataka viongozi kuendelea kuwa mbele ya matukio kwa kusikiliza na kutatua kero kabla hazijafikia hatua kubwa.

“Nimeona viongozi wa Mkoa wa Iringa wako mbele ya matukio. Kila hoja iliyojitokeza tayari ilikuwa imepokelewa na hatua mbalimbali zilikuwa zimeanza kuchukuliwa. Huo ndiyo mwelekeo ambao Serikali inautaka,” alisema.

Waziri Mkuu aliwataka viongozi wa Mkoa huo kufuatilia moja baada ya nyingine kero zote zilizowasilishwa katika ziara yake na kuhakikisha wananchi wanapata mrejesho wa hatua zinazochukuliwa.

Alisema Serikali itaendelea kufanya tathmini ya utekelezaji wa maelekezo hayo na kwamba viongozi wa mikoa na halmashauri wanapaswa kuweka kumbukumbu za utekelezaji wa kila hoja iliyowasilishwa na wananchi.

Katika sekta ya afya, Dkt. Mwigulu alisisitiza umuhimu wa kuhakikisha dawa muhimu na vifaa tiba vinapatikana kulingana na mahitaji ya maeneo husika pamoja na kuimarisha usimamizi wa fedha zinazotengwa kwa ajili ya huduma za afya.

Aidha, alizitaka halmashauri na taasisi za umma kuendelea kuwasaidia watu wenye ulemavu, wazee wasiojiweza na makundi mengine maalum kwa kutumia rasilimali zilizopo ili kuboresha ustawi wao.

Kwa upande wa miundombinu, Waziri Mkuu alielekeza kuharakishwa kwa utekelezaji wa miradi ya barabara iliyo katika hatua mbalimbali za maandalizi na utekelezaji huku akisisitiza ujenzi wa miundombinu yenye viwango vinavyoweza kuhimili changamoto za mazingira.

Pia aliwataka viongozi kuendelea kutatua migogoro ya ardhi kwa haki na kwa kuzingatia sheria pamoja na kuhimiza wananchi kurasimisha umiliki wa mali zao ili kuepusha migogoro inayoweza kujitokeza baadaye.

Akizungumzia utendaji wa watumishi wa umma, Dkt. Mwigulu alisema ni muhimu kuwatambua na kuwathamini watumishi wanaofanya kazi kwa uadilifu na ufanisi huku hatua stahiki zikichukuliwa kwa wale wanaoshindwa kutekeleza wajibu wao.

“Haki, uwajibikaji na huduma bora kwa wananchi lazima viwe msingi wa utendaji wetu. Wananchi wanatarajia kuona matokeo ya kazi zetu na ndiyo dhamira ya Serikali,” alisema.

Aidha, Waziri Mkuu aliwataka viongozi wa mkoa huo kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa maelekezo yote aliyoyatoa katika ziara hiyo ikiwemo migogoro ya ardhi, madai ya wananchi dhidi ya taasisi na kampuni mbalimbali, pamoja na masuala ya ustawi wa jamii yaliyowasilishwa katika mikutano ya hadhara.

Awali, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Kheri James alisema ziara ya Waziri Mkuu imeimarisha ari ya uwajibikaji kwa viongozi na watumishi wa umma pamoja na kutoa mwelekeo wa kushughulikia changamoto zinazowakabili wananchi katika maeneo mbalimbali ya Mkoa huo.











Mwamvua Mwinyi, Bagamoyo Juni 7,2026
JESHI la Polisi Mkoa wa Pwani limeanza uchunguzi wa kina kufuatia malalamiko ya mwanamke mmoja mkazi wa Gongo la Mboto, Dar es Salaam, anayodai kubadilishiwa mtoto baada ya kujifungua kwa njia ya upasuaji katika Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo.

Akitoa ufafanuzi kuhusu tukio hilo, kamanda wa Polisi mkoani Pwani,Salim Morcase alimtaja mlalamikaji huyo kuwa ni Filomena Richard Mataris (36), ambaye pamoja na mume wake, Carlos Kapata, walifika Kituo cha Polisi Bagamoyo Juni 5, 2026 na kutoa taarifa ya madai hayo.

Kwa mujibu wa Morcase, Filomena alihamia Kerege wilayani Bagamoyo Aprili 14, 2026 kwa ndugu yake Avetha Mabadiliko kwa ajili ya kupata uangalizi wa karibu wakati wa ujauzito.

"Mei 17, 2026 alipata uchungu wa kujifungua na kupelekwa Hospitali ya Kerege, ambapo baada ya kufanyiwa uchunguzi alibainika kuwa na dalili za uzazi pingamizi na kuhamishiwa Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo kwa ajili ya upasuaji."

" Mei 18, 2026 majira ya saa 8:30 usiku, Filomena alijifungua mtoto wa kiume kwa njia ya upasuaji na kudai kuwa alimwona na kumbeba mtoto huyo akiwa mzima wa afya, baada ya kuhamishiwa wodini, alidai kuoneshwa picha ya mtoto kupitia simu ya daktari na kuambiwa kuwa ndiye mtoto wake aliyefariki dunia.

Mama huyo alifafanua kuwa mtoto aliyeoneshwa kwenye picha alikuwa na changamoto mbalimbali za kiafya ikiwemo kichwa kilichobonyea na uvimbe kifuani, hali ambayo alisema ilikuwa tofauti na mtoto aliyemuona mara baada ya kujifungua.

Aidha, Filomena alidai kuwa aliambiwa mwili wa mtoto huyo ulikwishakabidhiwa kwa ndugu zake kwa ajili ya mazishi, bila yeye wala baba wa mtoto kushirikishwa au kufahamishwa kuhusu taratibu hizo.

Katika hatua za awali za uchunguzi, Kaimu Mganga Mkuu wa Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo, Dk. Mariam Ngwele, alieleza kuwa mtoto aliyezaliwa alikuwa na matatizo ya kiafya ikiwemo kichwa kilichobonyea, uvimbe kifuani na changamoto za upumuaji.

Dk. Ngwele, anasema mtoto huyo alifariki muda mfupi baada ya kuzaliwa licha ya jitihada za kitabibu zilizofanyika.

Na Mwandishi wetu, Mirerani 


MADINI ya Tanzanite ya thamani ya zaidi ya shilingi milioni 993 yameuzwa kwenye minada miwili iliyofanyika hivi karibuni katika jengo la Tanzanite Exchange Centre mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara.

Afisa madini mkazi Mirerani (RMO) George Kaseza, ameyasema hayo kwenye ziara ya Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo Kenani Laban Kihongosi alipotembelea jengo hilo na kukagua akiwa ameongozana na viongozi wa mkoa na wilaya.

Kaseza amesema minada miwili ilifanyika hivi karibuni ambapo mnada wa kwanza wa mabroka ulifanyika Mei 15 mwaka 2026 kwa washiriki 84 na madini ya shilingi 271,270,100 yalinunuliwa.

"Mnada wa pili wa dealers ulifanyika Mei 21 mwaka 2026 na madini ya thamani ya shilingi 721,750,000 yalinunuliwa," amesema RMO Kaseza.

Amesema jengo la Tanzanite Exchange Centre linamilikiwa na Halamshauri ya Wilaya ya Simanjiro ila linaendeshwa na Tume ya Madini kupitia ofisi yake.

Katibu wa NEC, Itikadi Uenezi na Mafunzo Kenani Laban Kilongosi amewapongeza watumishi wa ofisi ya RMO Mirerani kwa namna wanavyofanya kazi katika eneo hilo.

Kenani amesema tayari soko hilo limeanza kuonyesha matokeo chanya ya uwekezaji huo kutokana na mwitikio mkubwa wa wafanyabiashara na mafanikio ya minada iliyofanyika ndani ya muda mfupi tangu kuanza kutumika.


Na Mwandishi wetu – Dar es Salaam

SERIKALI kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) imeingia Makubaliano ya Ushirikiano (MoU) na Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam (DIT) yenye lengo la kuimarisha usimamizi wa maafa nchini kwa kutumia sayansi, teknolojia na ubunifu.

Akizungumza mapema hii leo (08 Juni, 2026) katika hafla ya utiaji saini wa makubaliano hayo Katibu Mkuu wa ofisi hiyo, Dkt. Jim Yonazi, amesema hatua hiyo ni utekelezaji wa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kujenga mifumo madhubuti ya kiutendaji inayoongozwa na maarifa, sayansi na teknolojia ikiwemo matumizi ya Akili Unde (AI) katika kukabiliana na maafa.

Amesema makubaliano hayo yanatekeleza pia mapendekezo ya Mkutano wa Nane wa Umoja wa Mataifa wa Jukwaa la Dunia la Upunguzaji wa Vihatarishi vya Maafa uliofanyika Geneva, Uswisi, mwezi Juni 2025, na yanaashiria mabadiliko ya kimkakati katika namna Serikali inavyoshughulikia changamoto za maafa kutoka mfumo wa kusubiri majanga hadi mfumo wa kujikita katika kinga, maandalizi na tahadhari.

“Vyuo vikuu na taasisi za utafiti, ikiwemo Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam, zina jukumu muhimu la kuzalisha maarifa na suluhisho za kisayansi zitakazosaidia kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa nchini,”amesema.

Ameongeza kuwa ili kuhakikisha utekelezaji madhubuti wa makubaliano hayo, Serikali itaandaa Mpango Kazi wa utekelezaji pamoja na Agenda ya Kitaifa ya Utafiti wa Usimamizi wa Maafa itakayobainisha maeneo ya kipaumbele yanayohitaji ufumbuzi wa kisayansi na kiteknolojia.

Dkt. Yonazi amesisitiza kuwa mafanikio ya makubaliano hayo yatapimwa kwa matokeo halisi yatakayochangia kuongeza usalama wa wananchi, kulinda rasilimali za taifa na kuimarisha ustahimilivu wa jamii dhidi ya maafa.

Ushirikiano huo unaendana na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayoweka msisitizo katika matumizi ya sayansi, teknolojia na ubunifu kama nguzo kuu ya maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii.

Kwa upande wake Mkuu wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam Prof.Preksedis Marco Ndomba amesema kuwa taasisi imeandika historia kwa kusaini hati ya ushirikiano na Ofisi ya Waziri Mkuu ambapo ameeleza kuwa mchakato huu ulianza muda mrefu na matunda yake yameanza kuonekana jambo ambalo ni mafanikio makubwa.

“Tunaahidi juu ya kufanikisha makubaliano hayo kwa kuwa, uwezo huo tunao, utalaam upo wa kutosha kwa kushirikiana kwenye masuala ya viatarishi kitaifa ili kufanikisha adhima hii ya Serikali,” Alisema Profesa Ndomba.













Bagamoyo, Juni 5, 2026.
HALMASHAURI ya Wilaya ya Bagamoyo imetoa wito kwa wadau wa maendeleo kuimarisha ushirikiano na serikali katika kuboresha miundombinu ya elimu na kuendeleza uhifadhi wa mazingira shuleni ili kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa wanafunzi.

Wito huo ulitolewa Alhamisi wakati wa zoezi la kupanda miti lililoandaliwa na Airtel Tanzania chini ya udhamini wa Airtel Africa Foundation katika Shule ya Msingi Kiromo iliyopo Wilayani Bagamoyo, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani.

Akizungumza kwa niaba ya Afisa Elimu wa Wilaya ya Bagamoyo, Hamis Kimenya ambaye ni Mkuu wa Kitengo cha Michezo, Utamaduni na Sanaa Halmashauri ya Mji wa Bagamoyo aliipongeza Airtel Tanzania kwa kushirikia na Airtel Africa Foundation kwa kuendelea kuisaidia Shule ya Msingi Kiromo na kuwahimiza wadau wengine wa sekta binafsi kujiunga na juhudi hizo zinazolenga kuboresha elimu na kulinda mazingira.

Alisema juhudi za uhifadhi wa mazingira, hasa upandaji miti, zinachangia kwa kiasi kikubwa kuboresha maeneo ya shule, kuongeza uoto wa kijani, kutoa kivuli, na kutengeneza mazingira yenye afya na yanayofaa zaidi kwa ujifunzaji.

“Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo inaendelea kujitolea kuweka mazingira wezeshi ya ushirikiano kati ya serikali na sekta binafsi, hasa katika sekta ya elimu. Tunahimiza wadau wengi zaidi kuunga mkono shule na jitihada za uhifadhi wa mazingira,” alisema.

Mkurugenzi Mtendaji wa Airtel Tanzania, Charles Kamoto, alisema Siku ya Mazingira Duniani inakumbusha ulimwengu kuwa ulinzi wa mazingira ni jukumu la pamoja linalohitaji hatua za pamoja kutoka kwa serikali, taasisi binafsi na jamii.

Alisema mpango wa kampuni hiyo wa kupanda miti katika Shule ya Msingi Kiromo unaonyesha dhamira yake ya muda mrefu katika uendelevu wa mazingira na maendeleo ya jamii.

“Leo hatupandi miti tu; tunawekeza katika mazingira yetu, jamii zetu, na vizazi vyajavyo,” alisema Kamoto. “Miti hii ya matunda itasaidia kulinda ardhi, kuboresha ubora wa hewa, kutoa kivuli, na baadaye kutoa matunda yatakayowanufaisha wanafunzi na jamii inayozunguka.”

Kamoto aliongeza kuwa mpango huo unaenda sambamba na maono ya Taasisi ya Airtel Africa (Airtel Africa Foundation) kupitia mpango wake wa “Adopt a School”, (Shule Yetu) ambao unasaidia uendelezaji wa mazingira salama, ya kijani, jumuishi na wezeshi ya kujifunzia kwa watoto kote Afrika.

Alibainisha kuwa Airtel imeendelea kuongeza juhudi za uhifadhi wa mazingira, akigusia kuwa mwaka jana kampuni hiyo ilifanya zoezi la kusafisha fukwe katika Fukwe ya Kawe jijini Dar es Salaam.

Mwaka huu, Airtel Tanzania imepanua juhudi zake kupitia upandaji miti katika Shule ya Msingi Kiromo, ikionyesha kuongezeka kwa dhamira ya uendelevu.

Katika hatua nyingine, mnamo Juni 5, 2026, Airtel pia ilifanya zoezi kubwa la kusafisha fukwe katika fukwe za Msasani na Kawe jijini Dar es Salaam kama sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani. Zoezi hilo lilisimamiwa na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC).

Akizungumza wakati wa usafi huo, Afisa Mazingira wa NEMC, Felician Kairuki aliwasihi wadau kuimarisha ushirikiano katika ulinzi wa mazingira kulingana na sera za kitaifa na mikakati ya usimamizi wa mazingira.

“Tunasisitiza umuhimu wa ushirikiano miongoni mwa wadau wote ili kuhakikisha mazingira yanalindwa kwa faida ya vizazi vya sasa na vijavyo,” alisema Kairuki.

Aliongeza kuwa ushirikiano endelevu kati ya taasisi za serikali, wadau wa sekta binafsi na jamii ni muhimu katika kukabiliana na changamoto za mazingira kama vile uchafuzi wa mazingira na usimamizi wa taka.

Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano wa Umma Airtel Tanzania, Jackson Mbando alisema kampuni hiyo imeendelea kutekeleza mipango mbalimbali ya uendelevu, ikiwa ni pamoja na kukuza suluhisho za kidijitali zinazopunguza utegemezi wa karatasi na vifaa vingine vinavyoweza kuchangia uharibifu wa mazingira.

Alisema hatua hizi ni sehemu ya dhamira pana ya Airtel ya kufanya biashara kwa masuala ya uwajibikaji na usimamizi wa mazingira.

Afisa Mtendaji wa Kata ya Kawe, Husna Nondo aliipongeza Airtel kwa kushiriki kikamilifu katika mazoezi ya kusafisha fukwe, akibainisha kuwa mamlaka za serikali za mitaa zinaendelea kuchukua hatua za kisheria dhidi ya watu binafsi na taasisi zinazochafua mazingira.

Alisisitiza kuwa ushirikiano kati ya serikali, sekta binafsi na jamii ni muhimu katika kuhakikisha kuwa fukwe, maeneo ya wazi na mazingira ya mijini yanabaki kuwa safi, salama na endelevu.

Mipango hiyo ya pamoja huko Bagamoyo na Dar es Salaam inaangazia ukuaji wa ushirikiano kati ya sekta binafsi, mashirika ya serikali na vyombo vya udhibiti katika kuendeleza uhifadhi wa mazingira, kukuza uendelevu na kuboresha ustawi wa jamii kote nchini Tanzania.
SAFARI ya miaka 30 ya mabadiliko katika sekta ya elimu nchini imeendelea kuandikwa na Dar es Salaam Independent School (DIS), shule iliyoanzishwa mwaka 1996 na Mama Susan L. Huxtable kwa lengo la kutoa elimu yenye viwango vya kimataifa kwa Watanzania, wakiwemo wale wenye uwezo wa kawaida wa kiuchumi.

Tangu kuanzishwa kwake, shule hiyo imekuwa ikitoa elimu kwa mtaala wa Cambridge huku ikijikita katika kuwajengea wanafunzi uwezo wa kufikiri, kufanya maamuzi na kujitegemea kupitia mchanganyiko wa masomo ya nadharia na vitendo.

Mkuu wa shule hiyo, Catherine Shindika, amesema mafanikio ya DIS yanaonekana kupitia wahitimu wake ambao wameendelea kufanya vizuri katika taasisi mbalimbali za elimu na maeneo ya kazi ndani na nje ya nchi.

Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa maadhhimisho ya miaka 30 ya shule hiyo, yaliyofanyika Mbweni campus Dar es Salaam, Shindika, ambaye amejiunga na shule hiyo mwaka 1998 na kuhudumu kwa miaka 28, alisema shule hiyo imeendelea kujijengea sifa kutokana na ubora wa wanafunzi wake.

“Shule yetu inatangazwa na wahitimu wetu. Wanapohamia shule nyingine au kuingia katika ajira, uwezo wao huwavutia walimu na waajiri kiasi cha kuhoji walikotoka. Huo ndiyo ushahidi wa ubora wa elimu tunayotoa,” alisema.

Aliongeza kuwa DIS imekuwa mfano wa kuigwa hata kwa mamlaka za elimu, akibainisha kuwa wakati wa ukaguzi wa serikali, maofisa kutoka Wizara ya Elimu walivutiwa na mfumo wa ukaguzi wa ndani wa shule hiyo na kujifunza baadhi ya mbinu zinazotumika.
Kwa upande wa wazazi, Monicha Nyangasa ambaye ana watoto wawili wanaosoma katika shule hiyo, alisema DIS imekuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya watoto wake kielimu na kijamii.

“Unaona mabadiliko ya watoto kila siku. Wamekua katika elimu, kujiamini na kujitambua. Kitu kizuri zaidi ni kwamba shule inashirikisha wazazi katika kila hatua, hivyo tunashuhudia maendeleo hayo moja kwa moja,” alisema.

Naye mzazi mwingine, Paul Bomani ambaye pamoja na kuwa na watoto wawili shuleni hapo yeye pia alihitimu kidato cha nne hapo hapo mwaka 1998 alisema shule hiyo imeweka mazingira yanayowakuza wanafunzi kuwa wabunifu na washiriki wa maamuzi yanayowahusu.

Alitolea mfano wa mchakato wa kuchagua sare za shule, ambapo wanafunzi walishiriki katika maonesho ya mitindo na kutoa maoni yaliyosaidia kupatikana kwa muonekano wa sare zinazotumika sasa.

“Hii inaonyesha namna wanafunzi wanavyopewa nafasi ya kufikiri, kubuni na kushiriki katika kufanya maamuzi. Ni sehemu ya kuwajenga kuwa viongozi wa baadaye,” alisema.

Kwa upande wa wanafunzi, Widad Hamis alisema mbali na masomo ya darasani, DIS imekuwa ikiwapa maarifa yanayowasaidia kuishi vizuri katika jamii na kukabiliana na mahitaji ya dunia ya sasa.

“Hapa tunajifunza namna ya kuishi na watu wengine, kujenga mahusiano mazuri na kutumia teknolojia katika maisha ya kila siku. Shule imewekeza sana katika kutufundisha teknolojia na kutuandaa kwa maisha ya baadaye,” alisema.

Kadiri DIS inavyoadhimisha miaka 30 tangu kuanzishwa kwake, shule hiyo inaendelea kuwa sehemu ya taasisi zilizochangia kukuza elimu ya kisasa nchini, huku ikijenga kizazi cha vijana wenye maarifa, ubunifu na uwezo wa kushindana katika mazingira ya kimataifa.






Na. Calvin Katera - Arusha.

Maonesho ya Karibu- KiliFair yameendelea kuwa na umuhimu mkubwa kwa TANAPA kwani ni jukwaa la kuwakutanisha wadau wa ndani na nje ili kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo katika Hifadhi za Taifa nchini. Kupitia maonesho hayo, TANAPA hukutana na wadau mbalimbali wa utalii wa ndani na nje ambao wameendelea kuwekeza na kuchagiza ongezeko la watalii katika Hifadhi za Taifa nchini.

Akifungua Maonesho hayo leo juni 05, 2026 katika Viwanja vya Magereza jijini Arusha, Mkurugenzi wa Utalii Dkt. Thereza Mugobi kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii alisema kuwa Karibu-KiliFair ni zaidi ya maonesho, vilevile ni uwekezaji wa kimkakati katika mustakabali wa utalii wa Tanzania. 

Uhusiano huu wa kibiashara ulioanzishwa katika jukwaa hili la Karibu KiliFair umezalisha ushirikiano mpya, kuongeza idadi ya watalii wanaowasili nchini, kuvutia uwekezaji, kutengeneza ajira, na kuimarisha maisha ya jamii zinazotegemea utalii. 

"Serikali itaendelea kuwekeza katika miundombinu ya utalii ikiwemo malazi, viwanja vya ndege, barabara ili kuboresha uzoefu wa watalii na kuwafikisha katika maeneo mbalimbali yenye vivutio kwa urahisi. Aidha, Wizara itaendelea kutangaza vivutio vyake kupitia njia za kidijitali ili kuyafikia masoko mbalimbali duniani." Alisema Dkt. Mugobi.

Naye, mwakilishi kutoka “TATO” Wilbard Chambulo, alisema kuwa maonesho haya ni daraja linalounganisha wadau wa ndani ambao ni mawakala wa utalii na waongoza watalii pamoja na mawakala wa kimataifa kutoka katika mabara yote duniani.

Sanjari na hayo Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi na Mkuu wa Kanda ya Kaskazini Dkt. Beatrice Kessy kwa niaba ya Kamishna wa Uhifadhi TANAPA aisema; “Karibu-KiliFair huimarisha ushirikiano kati ya TANAPA na wadau wa sekta ya utalii duniani. 

Kupitia mikutano na majadiliano ya kibiashara, TANAPA hujenga mahusiano mapya, hujifunza mwenendo na muelekeo wa masoko ya utalii na uwekezaji ili kupanua wigo wa uwekezaji na kukuza utalii nchini.”

Ushiriki wa TANAPA katika Karibu-KiliFair unaendelea kuwa chachu ya kutangaza vivutio vya utalii, kuimarisha ushirikiano na wadau wa sekta ya utalii, pamoja na kuvutia watalii na wawekezaji zaidi kutembelea na kuwekeza katika Hifadhi za Taifa Tanzania.



Kampuni ya HQ Tanzania imetoa msaada wa vifaa tiba kwa watoto wenye ulemavu wanaolelewa na Kituo cha SBHD Foundation, hatua inayolenga kusaidia ustawi na kuboresha maisha ya watoto wenye mahitaji maalum.

Akizungumza baada ya kupokea msaada huo, Mkurugenzi wa SBHD Foundation, Suma Geofrey, alisema vifaa hivyo vitasaidia kuimarisha huduma zinazotolewa kwa watoto hao na kuchangia katika juhudi za kuwawezesha kuishi kwa kujitegemea zaidi.

Alitoa shukrani kwa uongozi wa HQ Tanzania kwa mchango huo, akisema ushirikiano kati ya sekta binafsi na taasisi zinazohudumia makundi maalum una nafasi muhimu katika kuimarisha ustawi wa jamii.

Suma pia alitoa wito kwa wadau mbalimbali na wananchi kuendelea kushiriki katika kusaidia watoto wenye mahitaji maalum kupitia michango na huduma mbalimbali zinazoweza kuboresha mazingira yao ya maisha na kujifunzia.









Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Judith Kapinga, akiwa katika ziara ya kikazi nchini Uturuki Juni 06, 2026, Jijini Istanbul amefanya mazungumzo na Waziri wa Viwanda na Teknolojia wa Uturuki, Mehmet Fatih Kacır pamoja na Waziri wa Biashara wa Uturuki, Ömer Bolat, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi na viwanda kati ya nchi hizi mbili.

Mazungumzo na Waziri Kacır yamejikita katika kukuza maendeleo ya viwanda vya kimkakati, kuimarisha matumizi ya teknolojia, pamoja na kuhamasisha uwekezaji katika viwanda rafiki kwa mazingira.

Mhe. Kapinga ameeleza dhamira ya serikali ya kutumia ushirikiano huo kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya mwaka 2050 ya kuwa nchi ya kipato cha kati cha juu kupitia mageuzi ya sekta ya viwanda, huku Uturuki ikiahidi kuendeleza ushirikiano wa kiufundi, kiteknolojia na ubunifu kwenye sekta hiyo.

Kwa upande wa biashara, mazungumzo na Waziri Bolat yamejikita katika kuimarisha mazingira wezeshi ya uwekezaji na kuongeza kiwango cha biashara kati ya Tanzania na Uturuki, ambacho kwa sasa kimefikia takribani Dola za Marekani milioni 354 mwaka 2026, huku lengo likiwa ni kufikia Dola za Marekani bilioni moja.

Pande zote mbili zilikubaliana kuandaa Mkutano wa Tume ya Pamoja ya Biashara utakaofanyika nchini Tanzania mwaka 2026 ili kujadili kwa kina fursa za kibiashara na uwekezaji.

Waziri Kapinga ametumia fursa hiyo kuelezea maeneo ya kimkakati ya uwekezaji nchini Tanzania, yakiwemo viwanda vya chuma, dawa na vifaa tiba, chakula, pamoja na kongani za viwanda vya kijani (green industrial parks), akisisitiza umuhimu wa kuongeza thamani ya malighafi za kilimo na madini ili kukuza ajira na kuongeza mauzo ya bidhaa zilizochakatwa badala ya kuuza malighafi ghafi.

Serikali ya Uturuki imeahidi kuendeleza ushirikiano wa kimkakati na Tanzania kupitia ubadilishanaji wa teknolojia, ujuzi na kuhamasisha sekta binafsi kushiriki kikamilifu katika miradi ya maendeleo ya viwanda.

Aidha, Waziri Kapinga alifanya mazungumzo na Waziri wa Biashara wa Somalia, Gamal Hassan, ambapo walijadili umuhimu wa kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi kupitia biashara na uwekezaji ili kunufaika vema na fursa za soko la Afrika Mashariki. Vilevile, kupitia mazungumzo hayo Mawaziri hao wameazimia kuanzisha makongamano ya biashara yatakayozikutanisha taasisi za serikali, wafanyabiashara na sekta binafsi kujadili kwa pamoja masuala muhimu ya ushirikiano.

Kadhalika, Mawaziri hao walijadili umuhimu wa uanzishwaji wa safari za ndege kati ya Tanzania na Somalia kupitia Shirika la Ndege la Air Tanzania ili kurahisisha usafirishaji na kupanua mtandao wa biashara kati ya nchi hizi mbili. Waziri Kapinga alihitimisha mazungumzo hayo kwa kumshukuru Waziri Hassan na alimuhakikishia utayari wa Tanzania kuimarisha uhusiano na Somalia na aliwakaribisha wawekezaji kutoka nchini humo kuja kuwekeza Tanzania.














-Asema uaminifu unazidi kupungua

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka viongozi nchini wawaelimishe wananchi umuhimu wa kuandikishana mikataba wanapopeana ardhi badala ya kuendelea kufanya hivyo kwa kuaminiana.

"Viongozi mliopo hapa waambieni wananchi hivi sasa masuala ya ardhi wasifanye kwa kuaminiana, wawe wanaandikishana kwa mikataba na tena katika ofisi za kijiji ili watambulike," amesema. 

Ametoa wito huo leo (Jumapili, Juni 7, 2026) wakati akizungumza na viongozi wa kada mbalimbali wa mkoa wa Iringa katika kikao cha majumuisho ya ziara zake kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa huo, mjini Iringa. 

"Ninawasihi wananchi tusiogope kurasmisha mambo yetu kwa sababu uaminifu unaenda unapungua. Tunaporasmisha, tunaepusha migogoro siku za usoni," amesisitiza. 

Waziri Mkuu ametoa rai hiyo kutokana na wingi wa kero zinazojitokeza kwenye mikutano aliyoishaifanya na hasa kwenye sekta ya ardhi. 

Amewataka viongozi wanapotaka kufanya uendelezaji wowote nao pia wahakikishe wanawapa wananchi husika mikataba ili kulinda haki yao.

"Tusichukue maeneo ya watu bila kuwalipa fidia. Kama kuna uendelezaji ni lazima kuwe na mikataba rasmi. Wananchi wa eneo husika wapewe barua za kuonesha utwaaji huo wakati wakisubiri fedha za fidia zipatikane. Liwe ni eneo limetengwa kwa uwekezaji,  ujenzi wa barabara au shule, watu wapewe barua. Ardhi ni jambo rasmi ndiyo sababu presha ya matumizi inazidi kuongezeka."

Wakati huohuo, Waziri Mkuu amewataka watumishi wa umma wanapokuwa kazini wavae vitambulisho vyenye majina yao ili iwe rahisi kuwatambua.

"Watumishi wa umma wavae vitambulisho ili tuwatambue kwa urahisi wale wanaotukwamisha. Tusirasimishe uozo kwenye ofisi zetu. Zipo ofisi utakuta wanaofanya kazi ni asilimia 20 lakini wanaoenda kazini ni asilimia 80. Twendeni tuchape kazi na kila mmoja amsimamie aliyekabidhiwa chini yake."

Ametumia fursa hiyo kumpongeza Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Heri James,  Mwenyekiti wa CCM wa Mkoa huo, Daudi Yassin na viongozi wote kwa kusimamia vizuri shughuli za maendeleo ya mkoa wao.

"Hongereni sana kwa sababu mkoa wenu umetulia. Nimepita majimbo yote saba sijakutana na ghasia za kugombea nafasi za uongozi. Katika maeneo yote, watu wenu wanaongelea masuala ya maendeleo."

Amesema wakati wa ziara zake, kuna baadhi ya hoja ziliibuliwa na wananchi lakini viongozi wa wilaya na mkoa walikuwa tayari wameshachukua hatua na hata ilipobidi mtu asafirishwe hawakusita kufanya hivyo.

Waziri Mkuu alianza ziara za mkoa wa Iringa Mei 2, mwaka huu kwa kutembelea Halmashauri zote tano na majimbo yote saba kila alipopata nafasi za mwisho wa wiki na leo amefanya majumuisho ya ziara zake. 





Top News