Uharibifu wa Ziwa Victoria: Matokeo ya Shughuli za Kibinadamu Yaanza Kuonekana Wazi

Katika miaka ya karibuni, kumekuwa na ongezeko kubwa la shughuli za kibinadamu kandokando ya Ziwa Victoria, hali ambayo sasa imeanza kuleta athari zinazoonekana wazi katika mfumo wa ikolojia wa ziwa hilo.
Uchunguzi uliofanywa na Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO), ukiongozwa na Katibu Mkuu wake, Boniventura Mwalongo, umebaini changamoto kadhaa zinazolikumba ziwa hilo. Ziara hiyo ilifanyika katika eneo la Kigoto, Mwanza, kwa kushirikiana na Taasisi ya Haki za Binadamu (TAHURI).

Miongoni mwa changamoto zilizobainika ni pamoja na uwepo wa magugu vamizi, matumizi holela ya rasilimali za ziwa, pamoja na uchafuzi wa maji unaotokana na majitaka yasiyodhibitiwa.

Aidha, kupungua kwa kina cha maji kumetajwa kuwa matokeo ya moja kwa moja ya uharibifu wa maeneo ya kinga ya fukwe, jambo linalochangia kuongezeka kwa tope na mchanga ndani ya ziwa. Hali hii inaathiri kwa kiasi kikubwa mazalia ya samaki na kusababisha kupungua kwa uzalishaji wa rasilimali hiyo muhimu.

Wataalamu wanaonya kuwa endapo hali hii itaendelea, usalama wa chakula, ajira za wavuvi na uchumi wa maeneo yanayozunguka ziwa hilo vitakuwa hatarini.


Mbunge wa Jimbo la Namtumbo Dk Juma zuberi Homera Aprili 11, 2026, Amekabidhi rasmi magari mawili kwa Ofisi ya TANESCO wilayani Namtumbo, hatua inayolenga kuongeza ufanisi na kasi ya utoaji wa huduma ya umeme katika jimbo letu.

Kupatikana kwa magari haya ni sehemu ya juhudi endelevu za kuboresha miundombinu na kuimarisha upatikanaji wa huduma muhimu kwa wananchi, hususan katika maeneo ya vijijini na pembezoni.

Magari hayo yanatarajiwa kurahisisha shughuli za kiutendaji, ikiwemo usimamizi wa miradi ya umeme, matengenezo ya miundombinu, pamoja na kushughulikia changamoto za huduma kwa wakati.

Aidha Mh Mbunge Amepongeza TANESCO kwa jitihada zake madhubuti katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya umeme kwa uhakika, hatua ambayo inaendelea kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika maeneo mbalimbali.

"Ninawapongeza watumishi wa taasisi hiyo kwa kujituma kwao na kuwasihi kuyatunza vyema magari hayo ili yaweze kudumu na kutoa tija iliyokusudiwa. Matumizi sahihi ya rasilimali hizi ni muhimu katika kufanikisha azma ya kuwahudumia wananchi kwa ufanisi zaidi".









Timu ya mpira wa miguu ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki (NJE Sports) imepoteza kwa mabao 3–2 dhidi ya timu ya Ubalozi wa Umoja wa Ulaya katika mechi ya kirafiki iliyochezwa Aprili 11, 2026, kwenye Uwanja wa John Merlin, jijini Dodoma.

Akizungumza mara baada ya mchezo huo, Mgeni Rasmi ambaye ni Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mheshimiwa James Milya (Mb), amezipongeza timu zote mbili kwa kuonesha ushindani wa kirafiki na kudumisha mshikamano. Amesema michezo ya aina hiyo ina mchango mkubwa katika kuimarisha ushirikiano, urafiki na diplomasia kati ya taasisi na mataifa.

Ameongeza kuwa mechi hiyo ni sehemu ya juhudi za kukuza diplomasia ya michezo, sambamba na kuendeleza uhusiano mzuri uliopo kati ya Wizara na Ubalozi wa Umoja wa Ulaya.

Mchezo huo pia ulihudhuriwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Said Shaib Mussa, ambaye amesema kuwa pamoja na ushindani uliokuwepo uwanjani, lengo kuu la mchezo huo lilikuwa kuimarisha uhusiano kati ya pande husika, akisisitiza kuwa huo ndio ushindi mkubwa zaidi kuliko mabao.

Kwa upande wake, kiongozi wa timu ya Ubalozi wa Umoja wa Ulaya, Bw. Ally Mwinchade, amesema ameridhishwa na kiwango cha ushindani kilichooneshwa na timu zote mbili, akieleza kuwa mchezo huo umeimarisha zaidi uhusiano wa kirafiki kati ya pande hizo.

Ameongeza kuwa ushindi huo si matokeo ya uwanjani pekee, bali pia ni ishara ya mshikamano, ushirikiano na dhamira ya kuendeleza diplomasia kupitia michezo. Aidha, ameipongeza timu ya NJE Sports kwa kuonesha mchezo mzuri na kuahidi kuendeleza ushirikiano huo katika michezo ijayo.















Na Munir Shemweta, WANMM Nairobi

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt Leonard Akwilapo, amekutana na kufanya mazungumzo na Afisa Mtendaji Mkuu wa Shelter Afrique Bw. Thierno-Habib Hann jijini Nairobi, nchini Kenya.

Viongozi hao wawili wamekutana pembezoni mwa Kongamano la Miji Afrika (2nd Africa Urban Forum) lililofanyika kuanzia Aprili 8 hadi 10, 2026 nchini Kenya, na kukutanisha mataifa mbalimbali Barani Afrika kwa lengo la kubadilishana uzoefu na suluhisho bunifu katika kukabiliana na changamoto za maendeleo ya miji na makazi.

Dkt Akwilapo na Bw.Thierno-Habib Hann katika kikao chao walijadili masuala mbambali yanayohusu uimarishaji wa upatikanaji wa makazi nafuu kwa wananchi pamoja na ushirikiano kati ya serikali na taasisi za kifedha katika kufanikisha azma hiyo.

Shelter Afrique ni taasisi ya kifedha ya kimataifa inayolenga kusaidia maendeleo ya makazi Barani Afrika, huku makao makuu yake makuu yakiwa jijini Nairobi nchini Kenya.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (Kulia) akizungumza na Mtendaji Mkuu wa Shelter Afrique Bw.Thierno-Habib Hann jijini Nairobi, Kenya walipokutana pembezoni mwa Kongamano la pili la Miji Afrika (2ND Africa Urban Forum) lilofanyika nchini humo.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (Kushoto) na Mtendaji Mkuu wa Shelter Afrique Bw.Thierno-Habib Hann wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kikao chao jijini Nairobi, Kenya, walipokutana pembezoni mwa Kongamano la pili la Miji Afrika lilofanyika nchini humo.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (Kulia) akitambulishwa baadhi ya maafisa wa taasisi ya Shelter Afrique alipokutana na Mtendaji Mkuu wa taasisi hiyo Bw.Thierno-Habib Hann pembezoni mwa Kongamano la pili la Miji Afrika (2nd Africa Urban Forum) lilofanyika jijini Nairobi nchini Kenya. (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)

 



Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar,  Alhaj Hemed Suleiman Abdulla ametoa maelekezo kwa Taasisi zinazohusika na uratibu wa Ibada ya Hijja kwa mwaka 2026, kufanya mageuzi ya kimfumo ili kuboresha utoaji wa huduma kwa Mahujaji 4,029 kutoka Tanzania. 


Mhe. Abdullah amesema hayo katika Kikao kilichofanyika Visiwani Zanzibar leo ambapo amesisitiza umuhimu wa kuachana na mifumo ya kizamani na badala yake kuimarisha matumizi ya mifumo ya kidijitali.

Aidha, ameelekeza kuanzishwa kwa mfumo wa Kanzidata (database) utakaokuwa na taarifa sahihi za Mahujaji hao ili kurahisisha mipango na utoaji wa huduma.

Pia, amesisitiza umuhimu wa Taasisi hizo kuzingatia maslahi ya taifa kwa kuepuka migongano ya kimaslahi na kuhakikisha huduma zinatolewa kwa usawa. Ameeleza kuwa maelekezo hayo yanapaswa kuanza kutekelezwa mara moja ili kuhakikisha maandalizi ya msimu wa Hijja 2026 yanafanyika kwa ufanisi ili kuimarisha taswira ya nchi kimataifa.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Ayoub Mohammed Mahmoud amesema kuwa Wizara imeendelea kusaidia uratibu wa Hijja kupitia kitengo chake cha Usajili wa Jumuiya na imefanikisha upatikanaji wa hati za kusafiria kwa Mahujaji hao, kwa ufanisi mkubwa ili kuhakikisha zoezi hilo la Maandalizi ya Ibada linafanyika kwa ukamilifu

Naye, Waziri wa Kazi, Ajira na Mahusiano, Deus Sangu amesema Idadi ya Mahujaji imeendelea kuongezeka, kutokana na ongezeko hilo kumekuwa na changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika maandalizi na uratibu wa safari hizo. Hivyo, Serikali imeanza kufuatilia maandalizi hayo kwa lengo la kuweka miongozo bora itakayosaidia kuhakikisha wanapata huduma na maelekezo sahihi wanapoelekea kutekeleza Ibada hiyo.


 

Zaidi ya Watalii 90 wametembela Hifadhi ya Taifa Mkomazi kuvinjari na kufurahia utalii wa ndani leo Aprili 11, 2026 kufuatia ufunguzi wa tamasha la utalii lijulikanalo kama Same Utalii Festival msimu wa Tatu katika viwanja vya stendi wilayani Same, Mkoani Kilimanjaro.

Watalii hao walipata fursa ya kutembelea maeneo mbalimbali ya hifadhi ikiwemo Mbula, Kisima na Njiro na kujionea wanyamapori aina ya faru weusi, kivutio kinachowavutia wazawa na wageni lukuki toka nje na ndani ya mipaka ya Same kushuhudia ikolojia ya wanyama hao.

Akizindua rasmi tamasha hilo Waziri Mkuu (Mst.) wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyelitumikia Taifa kwa kipindi cha Awamu ya Nne kati ya mwaka 1990 hadi 1994 Mhe. John Malecela alisema kuwa matamasha haya ni kichocheo kikubwa cha utalii na hifadhi pia zina nafasi kubwa ya kuibua mazao mapya ya utalii yatakayochagiza kuongeza idadi ya watalii  kutembelea hii kwa kuwa na vionyo tofauti.

Aidha, Mhe. Malecela aliongeza kuwa utalii wetu uanze na sisi watanzania wenyewe ndani ya vivutio vyetu na hii ni kutokana na gharama nafuu zilizowekwa pamoja na uwezo mkubwa wa kufikia maeneo hayo kwa wepesi tofauti na wale wanaotoka maeneo ya mbali.

Naye, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii Mhe. John Mabula alieleza kuwa idadi ya watalii katika Hifadhi ya Taifa Mkomazi imeongeza kwa kiasi kikubwa kutoka 7800 kwa mwaka na kufikia 11000 kwa mwaka 2022 hadi 2026. Kadhalika alieleza kuwa uwepo wa vivutio na ongezeko la wageni ni fursa kwa wazawa kuweza kujiinua kibiashara na kuongeza kipato katika kaya zao.

Kwa, upande wake Mkuu Wilaya ya Same Mhe. Kasilda Mgeni alieleza kuwa Hifadhi ya Taifa Mkomazi iwape fursa vijana wa bodaboda kwa kutoa elimu ya kuongoza wageni ili wanapowapokea watalii waweze kuwakaribisha na kuwapa miongozo ya awali itakayochangia pato katika majukumu yao.

Hifadhi ya Taifa Mkomazi imekuwa moja ya kivutio pendwa katika  tamasha hili kwa kuwakutanisha wageni mbalimbali kutoka nje na ndani ya wilaya ya Same kutembelea wanyamapori adimu ikiwemo faru weusi, mbwa mwitu pamoja na uoto wa asili unaoipamba hifadhi hiyo. 













 



Na Oscar Assenga, Tanga

Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Tanga kimeeleza kuwa suluhisho la kudumu la kuboresha eneo la kuchezea katika Uwanja wa CCM Mkwakwani ni uwekaji wa nyasi bandia, huku wakipanga kushirikiana na wadau wa soka kufanikisha mpango huo.

Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua uwanja huo, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga, Rajab Abdurahman, alisema uwekaji wa nyasi bandia unakadiriwa kugharimu kati ya shilingi milioni 400 hadi 500.

Ziara hiyo ni sehemu ya ukaguzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo mkoani humo, ikiwemo ile inayotekelezwa kwa fedha zinazotolewa na Serikali chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa lengo la kupunguza kero kwa wananchi.

Abdurahman aliwataka viongozi wa CCM, ambao ni wamiliki wa uwanja huo, kutumia ubunifu na kushirikiana na wadau wa soka ili kuhakikisha wanapata fedha za kuweka nyasi bandia.

“Tutawaomba wadau wa soka nchini watakapohitajika kutusaidia, kwani dhamira yetu ni njema. Kama ambavyo wamekuwa wakitusaidia hapo awali, tunaamini watashiriki nasi kuhakikisha tunakuwa na uwanja wa kisasa zaidi,” alisema.

Alieleza kuwa maboresho ya uwanja huo yatasaidia kuinua uchumi wa Mkoa wa Tanga, kwani utaweza kutumika kwa mashindano ya kitaifa na kimataifa, ikiwemo CECAFA na michuano mingine ya Afrika.

“Tunapokuwa na uwanja mzuri, hata timu za nje zitakuja kucheza hapa Tanga. Hii itaongeza mzunguko wa fedha na kukuza uchumi wa mkoa wetu,” aliongeza.

Aidha, alikumbusha kuwa uwanja huo uliwahi kufungiwa kutokana na kutokidhi vigezo, hasa ubora wa eneo la kuchezea, akisisitiza kuwa hatua zinazochukuliwa sasa zinalenga kuhakikisha viwango vinazingatiwa kwa usalama wa wachezaji na ubora wa mchezo.

“Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) linapofungia uwanja si kwa kupenda, bali kuhakikisha viwango vinazingatiwa. Ndiyo maana tumekuwa wepesi kuchukua hatua za maboresho,” alisema.

Katika hatua nyingine, Abdurahman alieleza kuridhishwa na maendeleo ya ufungaji wa viti 6,500 vilivyotolewa na TFF chini ya Rais wake, Wallace Karia, licha ya kuwepo kwa ucheleweshaji mwanzoni.

Amesema tayari ameagiza kazi hiyo ikamilike ndani ya mwezi mmoja, na kwa sasa inaendelea vizuri chini ya usimamizi wa Mjumbe wa Kamati ya Siasa ya Mkoa, Nasoro Makau.

Kwa mujibu wa mpango huo, maeneo ya kipaumbele ni jukwaa kuu pamoja na sehemu za mashabiki wa klabu za Coastal Union na African Sports. Pia wameomba viti vingine 2,500 ili kukamilisha uwanja mzima.

Abdurahman aliishukuru Serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, inayoongozwa na Waziri Paul Makonda na Naibu wake Hamisi Mwinjuma, pamoja na Rais wa TFF Wallace Karia, kwa ushirikiano wao katika kuboresha uwanja huo.

Alisisitiza kuwa maboresho hayo yanalenga kuhakikisha klabu za Coastal Union na African Sports zinaendelea kucheza mechi zao za nyumbani mkoani Tanga badala ya kuhamishiwa maeneo mengine.

Aidha, aliwataka mashabiki wa soka kujitokeza kwa wingi uwanjani kuunga mkono timu zao.

“Haileti maana kuwa na uwanja mzuri halafu mashabiki wanabaki nyumbani kuangalia mechi,” alisisitiza.

Kwa upande wake, Meneja wa Uwanja wa Mkwakwani, Nasoro Makau, alisema hadi sasa wamefikia asilimia 40 ya ufungaji wa viti na wana uhakika wa kukamilisha kazi hiyo ndani ya mwezi mmoja.


Top News