FARIDA MANGUBE, KILOSA, MOROGORO
HOFU na simanzi vimetanda katika Kijiji cha Changarawe wilayani Kilosa mkoani Morogoro baada ya mwili wa mwanamke aliyeripotiwa kutoweka kwa zaidi ya miezi mitatu kugundulika ukiwa umefukiwa ndani ya nyumba aliyokuwa akiishi na rafiki yake wa kiume, ambaye naye hajulikani alipo.
Mwanamke huyo ametambuliwa kwa jina la Lilian Danstan Manga (27) ambaye aliripotiwa kutoweka tangu Desemba 11, 2025 katika Kitongoji cha Kipera, Kata ya Masanze.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, SACP Alex Mkama, mwili huo uligunduliwa baada ya mwanamke aliyekuwa akifanya usafi katika nyumba hiyo kubaini tuta la udongo ndani ya chumba.
“Baada ya taarifa hiyo kupokelewa, uchunguzi ulifanyika na hatimaye mwili wa mwanamke huyo kufukuliwa ndani ya nyumba hiyo,” alisema Mkama
Jeshi la polisi linamtafuta mtuhumuwa wa tukio hilo ambaye inaelezwa alikuwa akiishi na mwanamke huyo.
Baba wa marehemu, Danstan Albano Manga, amesema familia imepata pigo kubwa kufuatia tukio hilo.
Naye Felista Simon, jirani na mkazi wa Changarawe, amesema tukio hilo limewatia hofu wakazi wa eneo hilo.
“Hatukutarajia kabisa tukio la aina hii kutokea katika kijiji chetu,” alisema.
Kwa upande wake Nicholous Mkoma, Mwenyekiti wa Kijiji cha Changarawe, amesema viongozi wa kijiji walichukua hatua za haraka baada ya kupokea taarifa hizo na kushirikiana na vyombo vya usalama kufanikisha uchunguzi.




.jpeg)











.jpeg)

.jpeg)

































