BODI ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) inashiriki Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya 50 yanayoendelea kwenye Viwanja vya Sabasaba jijini Dar es Salaam, ikiwa ni jitihada za kuonyesha huduma mbalimbali zinazotolewa na Bodi hiyo pamoja na kutoa elimu kwa wananchi.

Banda la NBAA lipo ndani ya jengo la Wizara ya Fedha linawahudumia wananchi kwa kutoa maelekezo ya usajili wa mitihani katika ngazi mbalimbali za Taaluma ya Uhasibu, pamoja na kutoa maelekezo kuhusu ulipaji wa ada na huduma nyingine muhimu.

Katika kipindi hiki cha Sabasaba Bodi imewasogezea wananchi huduma karibu kwa kutoa huduma zote kama vile usajili wa watahiniwa wa mitihani ya Bodi, usajili wa wanachama wa ngazi mbalimbali, usajili wa Makampuni, usajili wa kozi mbalimbali zinazoendeshwa na Bodi.

Aidha, NBAA kwa sasa inatumia mifumo ya kidijitali kutoa huduma zake, ambapo wananchi wanaweza kufikia huduma hizo kupitia tovuti rasmi ya Bodi ambayo ni www.nbaa.go.tz.

Maonesho haya ya Sabasaba ni fursa kubwa kwa Bodi ya NBAA kuwasiliana moja kwa moja na wananchi na wadau mbalimbali wa taaluma ya uhasibu na ukaguzi, ili kuboresha utoaji wa huduma na kuelimisha kuhusu umuhimu wa taaluma hiyo katika maendeleo ya taifa.
Wafanyakazi wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) wakiwa kwenye picha ya pamoja katika banda la Bodi hiyo lililopo ndani ya jengo la Wizara ya Fedha.
Huduma zikiendelea kwenye banda la NBAA
TANZANIA imeendelea kupiga hatua katika sekta ya afya baada ya kuanza kutumika kwa kipimo kipya cha Checkfor UTI Test, kinachomwezesha mtu kujipima akiwa nyumbani ili kubaini uwezekano wa maambukizi ya njia ya mkojo (UTI).

Akizungumza hivi karibuni jijini Dar es Salaam, Dkt. Eshton Nkala alisema maambukizi ya UTI ni miongoni mwa changamoto za kiafya zinazowakumba watu wengi, huku dalili zake zikijumuisha kukojoa mara kwa mara, maumivu au muwasho wakati wa kukojoa, maumivu ya chini ya tumbo na mkojo kubadilika rangi au kuwa na harufu isiyo ya kawaida.

Alisema changamoto kubwa imekuwa ni kuchelewa kutambua dalili na kufika katika vituo vya afya, wakati utambuzi wa mapema husaidia kupunguza uwezekano wa maambukizi kuongezeka, kujirudia au kusababisha madhara zaidi kiafya.

Kwa mujibu wake, Checkfor UTI Test humsaidia mtu kupata taarifa za awali kuhusu uwezekano wa kuwa na UTI akiwa nyumbani, lakini hakichukui nafasi ya daktari wala hospitali, bali humwezesha mtumiaji kuchukua hatua mapema na kufika kituo cha afya kwa ushauri wa kitaalamu, vipimo zaidi na matibabu stahiki.

Dkt. Nkala alisema kipimo hicho kinazalishwa nchini na kampuni ya Canadian Biotech, hatua inayoonyesha mchango wa viwanda vya ndani katika uzalishaji wa vifaa tiba vinavyosaidia jamii kujitambua mapema na kuchukua hatua kwa wakati.

Aliongeza kuwa Checkfor UTI Test kinapatikana kupitia JD Pharmacy, Bariki Pharmacy na Cugra General Supplier, huku akisisitiza kuwa wananchi hawapaswi kupuuza dalili za UTI, bali wajitambue mapema na kutafuta matibabu sahihi kwa wakati.


Na Karama Kenyunko Michuzi Tv
MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Tundu Lissu ameiomba Mahakama ya Rufani kutupilia mbali maombi ya marejeo yaliyowasilishwa na Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP), akidai hayana msingi wa kisheria na yanalenga kuchelewesha usikilizwaji wa kesi ya tuhuma za uhaini inayomkabili.

Lissu alidai hayo mbele ya jopo la majaji watatu wa Mahakama ya Rufani baada ya Jamhuri kufungua shauri la mapitio kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu uliotupilia mbali notisi ya Jamhuri ya kuwasilisha ushahidi mpya katika kesi hiyo.

Alidai uamuzi wa Mahakama Kuu wa Februari 24, 2026 haukumaliza kesi ya msingi ya uhaini, hivyo ni uamuzi mdogo usioruhusiwa kukatiwa rufaa wala kuwasilishwa maombi ya marejeo kwa mujibu wa Sheria ya Mamlaka ya Rufani.

Lissu pia alidai DPP hakupaswa kuwasilisha maombi hayo moja kwa moja Mahakama ya Rufani bali alitakiwa kwanza kuandika barua rasmi kwa Jaji Mkuu.

Kwa upande wa Jamhuri, Wakili wa Serikali Mkuu Nassoro Katuga na Job Mrema waliieleza Mahakama kuwa Lissu ametegemea kanuni za mashauri ya madai badala ya jinai na kwamba maombi ya DPP yamewasilishwa kwa mujibu wa Sheria ya Mahakama ya Rufani na Kanuni zake.

Katuga alidai Mahakama Kuu ilikataa ushahidi huo kabla haujapokelewa na kupimwa, jambo ambalo lilinyima Jamhuri haki ya kusikilizwa kikamilifu, huku akisisitiza kuwa Mahakama ilipaswa kuangalia uhalali wa notisi ya kuongeza ushahidi.

Mrema naye alidai pingamizi la awali la Lissu halina uwezo wa kuondoa shauri lote na kwamba halijazingatia sheria ya sasa kwa kuwa linahusu mashauri ya madai.

Katika majibu yake, Lissu aliiomba Mahakama itupilie mbali maombi hayo na iamuru DPP amlipe fidia kwa kile alichodai ni ucheleweshaji wa makusudi wa shauri lake, akisema amekaa gerezani kwa mwaka mmoja na miezi mitatu huku kesi ikicheleweshwa kwa siku 139.

Katuga alipinga madai hayo akieleza kuwa maombi hayo hayajalenga kuchelewesha kesi na kwamba Mahakama ya Rufani ina mamlaka ya kuhakikisha mwenendo wa Mahakama Kuu unafuata sheria.

Baada ya kusikiliza hoja za pande zote, Mahakama iliahirisha shauri hilo hadi itakapotoa uamuzi wake kwa tarehe ambayo pande zote zitajulishwa.




Waziri wa Fedha Balozi Khamis Mussa Omary akipata maelezo kutoka kwa Mtakwimu Mkuu wa Serikali, Dkt. Amina Msengwa wakato alipotembelea katika Banda la Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) wakati alipotembelea banda hilo katika maonesho ya 50 ya Biashara Kimataifa yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (Sabasaba) jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Fedha Balozi Khamis Mussa Omary akipata maelezo wakati Maktaba mtandao YA NBS jinsi inavyofanya kazi ambapo wadau mbalimbali wanaweza kupata machapisho ya Kitakwimu alipotembelea katika Banda la Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) kwenye maonesho ya 50 ya Biashara Kimataifa yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (Sabasaba) jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Fedha Balozi Khamis Mussa Omary akizungumza katika Banda la Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) wakati alipotembelea banda hilo katika maonesho ya 50 ya Biashara Kimataifa yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (Sabasaba) jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Fedha Balozi Khamis Mussa Omary akipata maelezo kutoka kwa Kamishina wa Sensa ,Spika Mstaafu Anna Makinda wakati Waziri huyo alipotembelea katika Banda la Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) wakati alipotembelea banda hilo katika maonesho ya 50 ya Biashara Kimataifa yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (Sabasaba) jijini Dar es Salaam.


Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

MIXX imewakutanisha wajasiriamali 18 katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba), ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuwawezesha kutangaza bidhaa na huduma zao pamoja na kupanua masoko.


Akizungumza katika maonesho hayo, Mkuu wa Kanda ya Kusini ya Dar es Salaam wa MIXX by YAS, Robert Kasulwa, alisema wajasiriamali hao ni wanufaika wa awamu ya pili ya mradi wa Anzia Ulipo, unaolenga kuwawezesha Watanzania kujikwamua kiuchumi kupitia ujasiriamali.

Kasulwa alisema katika awamu hiyo, jumla ya wajasiriamali 48 wamenufaika na mafunzo pamoja na uwezeshaji wa biashara, huku 18 kati yao wakipata nafasi ya kushiriki maonesho ya Sabasaba ili kutangaza bidhaa zao na kukutana na wateja pamoja na wadau mbalimbali wa biashara.

Alieleza kuwa lengo la mradi huo ni kuwafikia Watanzania wengi zaidi na kuwainua kiuchumi kwa kuwajengea uwezo wa kuanzisha na kukuza biashara endelevu katika maeneo mbalimbali nchini.

"MIXX by YAS inaendelea kushirikiana na wajasiriamali kwa kuwapa fursa za kujifunza, kuonyesha bidhaa zao na kupanua mtandao wa biashara. Tunaamini uwezeshaji huu utachochea ukuaji wa uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla," alisema Kasulwa.

Aliongeza kuwa kampuni hiyo itaendelea kutekeleza programu mbalimbali za uwezeshaji wa wananchi kwa lengo la kuongeza ushiriki wa Watanzania katika shughuli za kiuchumi na kutumia huduma za kifedha za kidijitali kukuza biashara zao.







Na Mwandishi Wetu - Dar es Salaam.


Kadri Maonesho ya 56 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) yanavyoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) imeendelea kuthibitisha kuwa teknolojia ya nyuklia siyo teknolojia ya kutumika kwenye uzalishaji wa nishati pekee, bali ni nyenzo muhimu inayochochea maendeleo ya kiuchumi, biashara, uwekezaji na ustawi wa jamii kupitia matumizi yake katika sekta mbalimbali za maendeleo.

Leo ikiwa ni siku ya sita tangu kuanza kwa maonesho hayo yaliyofunguliwa rasmi tarehe 28 Juni na yanayotarajiwa kuhitimishwa tarehe 13 Julai 2026, banda la TAEC limeendelea kuwa moja ya maeneo yanayovutia idadi kubwa ya wananchi, wanafunzi, watafiti, wawekezaji, wafanyabiashara na wadau kutoka ndani na nje ya nchi wanaotaka kupata uelewa kuhusu nafasi ya teknolojia ya nyuklia katika maendeleo ya Tanzania.

Ushiriki wa TAEC katika maonesho haya unaendana na dhamira ya Serikali ya kuhakikisha wananchi wanapata elimu sahihi kuhusu matumizi salama ya mionzi na teknolojia ya nyuklia pamoja na mchango wake katika kukuza uchumi wa taifa kupitia uzalishaji wenye tija, huduma bora za afya, usalama wa chakula, maendeleo ya viwanda, utafiti na uhifadhi wa mazingira.

Akizungumza katika banda la TAEC lililopo ndani ya Banda Kubwa la China, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano wa TAEC, Bwana Peter Ngamilo, amesema maonesho ya Sabasaba ni jukwaa muhimu linaloiwezesha TAEC kuwasiliana moja kwa moja na wananchi na wadau mbalimbali, kuwaelimisha kuhusu majukumu ya Tume pamoja na fursa zinazotokana na matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika maendeleo ya Taifa.

“Lengo letu kubwa ni kuhakikisha wananchi wanafahamu kuwa teknolojia ya nyuklia ni nyenzo muhimu ya maendeleo. Kupitia maonesho haya tunaendelea kutoa elimu kuhusu matumizi salama ya mionzi, wajibu wa TAEC katika usimamizi na udhibiti wa matumizi ya mionzi nchini, pamoja na namna teknolojia hii inavyochangia kukuza biashara, kuongeza tija katika uzalishaji na kuboresha maisha ya wananchi,” amesema Bwana Ngamilo.

Ameeleza kuwa wananchi wengi wamekuwa wakitembelea banda la TAEC kwa lengo la kupata ufafanuzi kuhusu teknolojia ya nyuklia na matumizi yake katika sekta mbalimbali, hali inayoonyesha kuwa uelewa wa jamii kuhusu teknolojia hiyo unaendelea kuongezeka siku hadi siku.

Katika sekta ya afya, TAEC imekuwa ikiendelea kutoa elimu kuhusu matumizi ya mionzi katika uchunguzi wa magonjwa, tiba ya saratani, tiba za nyuklia na uchunguzi wa kitaalamu unaowezesha madaktari kutoa huduma zenye usahihi zaidi kwa wagonjwa. Matumizi haya yameendelea kuboresha ubora wa huduma za afya nchini na kuongeza uwezo wa taasisi za tiba kutumia teknolojia za kisasa katika kuokoa maisha ya wananchi.

Kwa upande wa kilimo, wananchi wanaelimishwa namna teknolojia ya nyuklia inavyosaidia kuboresha mbegu za mazao, kuongeza uzalishaji, kudhibiti wadudu waharibifu wa mazao, kuhifadhi chakula baada ya kuvunwa na kuongeza usalama wa chakula. Teknolojia hizi zinachangia kuongeza ushindani wa bidhaa za kilimo katika masoko ya ndani na nje ya nchi.

Katika sekta ya mifugo, TAEC inaendelea kuhamasisha matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika utambuzi wa magonjwa ya mifugo, kuboresha uzalishaji wa mifugo, kuimarisha lishe ya wanyama na kusaidia programu za uzalishaji zinazoongeza tija kwa wafugaji.

Sekta ya viwanda nayo ni miongoni mwa maeneo yanayonufaika kwa kiwango kikubwa kupitia matumizi ya teknolojia ya nyuklia. Kupitia teknolojia za mionzi, viwanda vinaweza kufanya ukaguzi wa ubora wa bidhaa bila kuziharibu (Non-Destructive Testing), kupima unene wa bidhaa mbalimbali, kufanya vipimo vya ubora wa miundombinu, kutambua hitilafu katika mitambo na kuongeza usalama wa uzalishaji. Teknolojia hizi husaidia kupunguza gharama za uzalishaji, kuongeza ubora wa bidhaa na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Aidha, katika sekta ya nishati na utafiti, TAEC inaendelea kushirikiana na taasisi mbalimbali za kitaifa na kimataifa kujenga uwezo wa matumizi ya teknolojia za nyuklia katika tafiti zinazolenga kutatua changamoto za maendeleo, usimamizi wa rasilimali za maji, ulinzi wa mazingira na matumizi bora ya maliasili.

Kwa mujibu wa Bwana Ngamilo, elimu inayotolewa katika maonesho haya pia inalenga kuondoa dhana potofu ambazo baadhi ya wananchi wamekuwa nazo kuhusu teknolojia ya nyuklia.

“Wananchi wengi walikuwa wakihusisha teknolojia ya nyuklia na silaha pekee, lakini wanapofika katika banda letu wanajionea ushahidi kuwa teknolojia hii inagusa maisha yao ya kila siku kupitia huduma za afya, uzalishaji wa chakula, maendeleo ya viwanda, utafiti, usimamizi wa mazingira na sekta nyingine nyingi zinazochochea maendeleo ya uchumi wa Taifa.”

Maonesho ya Sabasaba yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kuunganisha taasisi za Serikali, sekta binafsi, wawekezaji na wananchi katika kuonesha bidhaa, huduma na ubunifu unaochochea biashara na maendeleo ya uchumi wa Tanzania. Ushiriki wa TAEC katika maonesho hayo unaonesha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha teknolojia ya nyuklia inatumika kwa amani, usalama na manufaa ya wananchi wote huku ikichangia utekelezaji wa dira ya maendeleo ya taifa kupitia sayansi, teknolojia na ubunifu.

TAEC inaendelea kuwakaribisha wananchi wote kutembelea banda lake lililopo ndani ya Banda Kubwa la China, Vyumba Na. 60 na 61, katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Barabara ya Kilwa, Dar es Salaam, ili kujionea teknolojia mbalimbali zinazotumiwa nchini na kupata elimu kuhusu mchango wa teknolojia ya nyuklia katika kujenga uchumi imara, kuongeza ushindani wa biashara na kuharakisha maendeleo endelevu ya Tanzania.



Waziri wa Fedha Balozi Khamis Mussa Omary akipata maelezo katika Banda la Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) wakati alipotembelea banda hilo katika maonesho ya 50 ya Biashara Kimataifa yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (Sabasaba) jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Fedha Balozi Khamis Mussa Omary akikabidhiwa mfuko uliowekewa taarifa mbalimbali za Taasisi  katika Banda la Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) wakati alipotembelea banda hilo katika maonesho ya 50 ya Biashara Kimataifa yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (Sabasaba) jijini Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Msumbiji, Mheshimiwa Daniel Francisco Chapo baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kikazi, tarehe 03 Julai, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Msumbiji, Mheshimiwa Daniel Francisco Chapo akisaini Kitabu cha Wageni baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kikazi, tarehe 03 Julai, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Msumbiji, Mheshimiwa Daniel Francisco Chapo baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kikazi, tarehe 03 Julai, 2026.

 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Msumbiji, Mheshimiwa Daniel Francisco Chapo Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kikazi, tarehe 03 Julai, 2026.



 Waziri wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Dennis Londo, ametembelea banda la Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji katika maonesho ya Sabasaba 2026 na kupata maelezo kuhusiana na Majukumu na utendaji kazi wa Ofisi hiyo na kukabidhiwa Mfuko wenye ujumbe wa Dira 2050 Wekeza Tanzania.

Aidha, Naibu Waziri Dennis Londo amepongeza utendaji kazi wa Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji ikiwa ni pamoja na kuhamasisha uwekezaji na kuanza kwa utekelezaji wa Dira 2050 ikiwa ni injini ya kukuza uchumi wa Nchi.

Waziri wa Fedha Balozi Khamis Mussa Omary Akizungumza  katika Banda la Chuo cha  Uhasibu Arusha (IAA) wakati alipotembelea banda hilo katika maonesho ya 50 ya Biashara Kimataifa yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (Sabasaba) jijini Dar es Salaam.

Kamishina wa Sensa ,Spika Mstaafu Anna Makinda akisaini Kitabu katika Banda la Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA)  wakati alipotembelea banda hilo katika maonesho ya 50 ya Biashara Kimataifa yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (Sabasaba) jijini Dar es Salaam.


*Yawahimiza wananchi kutembelea banda

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
BARAZA la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET) limewahimiza wananchi kutembelea banda lake katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) ili kujionea mafanikio makubwa yaliyopatikana katika utekelezaji wa elimu ya amali na mafunzo ya ufundi stadi nchini.

Banda hilo limekuwa kivutio kutokana na uwepo wa wanafunzi kutoka shule za sekondari zenye mkondo wa amali, ambao wanaonesha kwa vitendo ujuzi, ubunifu na maarifa waliopata kupitia masomo yao.

Wanafunzi hao wanawasilisha kazi mbalimbali zinazoonyesha namna elimu hiyo inavyowaandaa kujiajiri, kuajirika na kuendelea na masomo ya juu wakiwa na msingi imara wa taaluma.

Mbali na maonesho ya vitendo, wataalamu wa NACTVET wanatoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu ya Baraza katika kusimamia ubora wa elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi, pamoja na kueleza fursa za masomo zinazopatikana katika vyuo vinavyosimamiwa na Baraza.

Pia wananchi wanapatiwa maelezo kuhusu taratibu za udahili, matumizi ya Namba ya Utambuzi na Tuzo (AVN), upatikanaji wa hati za matokeo na huduma nyingine zinazotolewa na Baraza kwa lengo la kuboresha utoaji wa elimu nchini.

Akizungumza katika maonesho hayo, mwanafunzi wa Kidato cha Tatu katika Shule ya Sekondari Baobab, Careen Maki, alisema mkondo wa amali umemjengea uwezo na kujiamini katika kufikia ndoto yake ya kuwa mhandisi wa umeme.

Alisema kwa sasa anasomea fani ya umeme kupitia mkondo wa amali, jambo ambalo linampa msingi mzuri wa kuendelea na elimu ya juu na kutimiza malengo yake ya kitaaluma.

Kwa upande wake, mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Bwiru mkoani Mwanza, Daud Elias, alisema anasomea fani ya ujenzi kupitia mkondo wa amali na anaamini elimu hiyo itamwezesha kutimiza ndoto yake ya kuwa Mhandisi wa Majengo.

Alieleza kuwa utofauti wa mkondo wa amali ni kwamba unampa mwanafunzi nafasi ya kujifunza kwa vitendo zaidi kuliko nadharia, hali inayoongeza uelewa, kujiamini na uwezo wa kutatua changamoto zinazohusiana na taaluma husika.

NACTVET imesema maonesho ya Sabasaba ni jukwaa muhimu kwa wazazi, wanafunzi, walimu, waajiri na wadau mbalimbali kujifunza kuhusu mchango wa elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi katika kuzalisha wataalamu wenye ujuzi, kukuza ubunifu, kuongeza ajira na kuchochea maendeleo ya uchumi wa Taifa.NACTVET yaonesha mafanikio ya elimu ya amali Sabasaba



Na Mwandishi wetu,

Wakulima wa zao la Korosho  wamemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kuwapatia pembejeo za kilimo licha ya uwepo wa changamoto mbalimbali.

Wakulima hao ambao ni Wakulima wa Korosho wa mkoa wa Mtwara wameendelea kupokea pembejeo za kilimo ikiwemo dawa za maji na dawa ya unga ama Sulphur ambapo hawakusita kupaza sauti zao za pongezi.

"Sisi Wakulima tunatambua jitihada za Rais Samia kutupa pembejeo ambapo hatujaamini kama tungepata kutokana na namna Wakubwa huko Ulaya wanavyopigana vita na hivyo kupelekea uzalishaji kupungua na kupata huku dawa ni Maajabu ambayo Rais Samia ameonyesha namna anavyotupambania sisi Wakulima." alisema Mwananchi ambaye pia ni Mkulima Ndugu Rashid Hamid maarufu kwa jina la Mkapa mkazi wa Nansinji.

Hayo yamejili wakati wa ziara aliyofanya Ndugu Emmanuel Shilatu ambaye ni Afisa Tarafa kujiridhisha juu ya mwenendo wa ugawaji wa pembejeo ambapo zoezi limeendelea vyema.

"Kwa niaba ya Wananchi ningependa kuungana nao kumpongeza Mhe. Rais Samia kwa namna anavyowajali Wakulima kwa kuwapatia pembejeo za kilimo. Anayafanya hayo sanjali na kuwapatia Wataalamu wa kilimo, kuwapatia mbegu na kuwasimamia Wakulima kupata masoko ya mazao Yao kupitia mfumo wa stakabadhi ghalani. Hauwezi kuongelea mafanikio ya Kilimo na Wakulima nchini pasipo kumtaja Rais Samia." Alisema Shilatu 

Halikadhalika Mwenyekiti Kijiji Cha Kivukoni Ndugu Jackson Joseph Milanzi alishukuru kwa pembejeo na kuhaidi kutekeleza maelekezo ya Afisa Tarafa ya kuendelea kusimamia ugawaji wa pembejeo hizo kwa uwazi, haki na usawa kama zoezi linavyoendelea.

Wakulima wa Korosho nchini wameanza kupokea pembejeo za kilimo mapema sana kwa msimu huu tofauti na hapo awali na hivyo wanatarajia kuwa na msimu mzuri wa Korosho kwa mwaka huu na hivyo kupata tija ya uzalishaji.






Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) imesema ushiriki wake katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam Sabasaba unalenga kutoa elimu ya uhifadhi wa wanyamapori, kuhamasisha utalii wa ndani, pamoja na kusogeza huduma kwa wananchi kupitia maonesho ya wanyamapori na uuzaji wa nyara halali za wanyamapori na nyama pori.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam Julai 3, 2026, Mhifadhi Mkuu wa TAWA, Steven Madenge, amesema wananchi wanaotembelea banda la mamlaka hiyo wanapata fursa ya kujionea wanyamapori mbalimbali wakiwemo twiga, simba, chui, fisi, pundamilia, tembo na mamba, hatua inayolenga kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa uhifadhi na kuwavutia kutembelea hifadhi za wanyamapori nchini.

Aidha, amewataarifu wananchi kuwa TAWA imeandaa programu mpya iitwayo Pande Marathon, inayotarajiwa kufanyika Agosti 1, 2026 katika Hifadhi ya Pande, jijini Dar es Salaam, amesema mbio hizo zinalenga kuimarisha afya pamoja na kuendelea kuunganisha wananchi na shughuli za utalii na uhifadhi nchini.









Na Mwandishi Wetu

Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) imesema imejipanga kutumia Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) kutoa elimu kwa wananchi kuhusu haki za binadamu na utawala bora pamoja na huduma mbalimbali zinazotolewa na tume hiyo.

Akizungumza katika banda la Tume hiyo kwenye maonesho hayo, Mkurugenzi wa Sheria wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Ellen Ruyage, alisema wananchi wanaotembelea banda hilo wanapata fursa ya kufahamu majukumu ya tume, kuwasilisha malalamiko yanayohusu ukiukwaji wa haki za binadamu na misingi ya utawala bora, pamoja na kupata ushauri na msaada wa kisheria.

Alisema tume inapokea malalamiko yote yanayohusu uvunjifu wa haki za binadamu na ukiukwaji wa misingi ya utawala bora, kisha kuyafanyia kazi kwa mujibu wa sheria, huku ikitoa maelezo kwa walalamikaji kuhusu hatua zinazochukuliwa.

"Tunapokea malalamiko yote yanayohusiana na uvunjifu wa haki za binadamu na ukiukwaji wa misingi ya utawala bora.

Aidha, tunatoa huduma za msaada wa kisheria pamoja na elimu kuhusu haki za binadamu na utawala bora ili wananchi wajue haki zao na namna ya kuzidai," alisema Ruyage.

Alifafanua kuwa si kila mwananchi anayewasilisha malalamiko yake hukumbana na ukiukwaji wa haki za binadamu au misingi ya utawala bora, bali wakati mwingine tatizo linaweza kuwa nje ya mamlaka ya tume. Hata hivyo, alisema tume huwapa mwongozo wa mahali sahihi pa kupata huduma ili kuhakikisha haki zao hazicheleweshwi.

Ruyage alisema juhudi za tume za kuendelea kutoa elimu zimeongeza uelewa wa wananchi, hali inayowafanya kujitokeza kwa wingi kuripoti matukio ya ukiukwaji wa haki zao na pale wanapoona misingi ya utawala bora haifuatwi.

Aliongeza kuwa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora inaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa ndani na nje ya nchi, ikiwemo mashirika ya kimataifa, hatua ambayo imewezesha huduma zake kuwafikia wananchi wengi zaidi katika maeneo mbalimbali nchini.

Aidha, alitoa wito kwa wananchi kutumia fursa ya maonesho ya Sabasaba kutembelea banda la tume ili kupata elimu, ushauri wa kisheria na kuwasilisha changamoto zozote zinazohusu haki za binadamu na utawala bora.

"Tume yetu iko wazi kwa wananchi wote. Tunawahimiza wajitokeze kupata huduma na elimu ili kujenga jamii inayozingatia haki za binadamu na misingi ya utawala bora," alisisitiza

Top News