Maafisa Biashara kutoka Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma leo tarehe 1 Julai, 2026 wametembelea Banda la Halmashauri ya Jiji la Dodoma katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba) yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam.

Wakiwa katika banda hilo, maafisa hao walipata maelezo kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa na Halmashauri ya Jiji la Dodoma, ikiwemo ushauri na miongozo kwa wananchi na wawekezaji kuhusu upatikanaji wa maeneo ya uwekezaji na huduma za ardhi, fursa za biashara katika sekta za kimkakati zinazokuwa kwa kasi pamoja na taratibu za uwekezaji ndani ya jiji

Akizungumza baada ya kutembelea banda hilo, Mkuu wa Divisheni ya Biashara, Viwanda na Uwekezaji kutoka Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro, Lusajo Mwasongwe alisema kuwa wamejifunza mambo mbalimbali yanayoweza kuwasaidia kuboresha utoaji wa huduma katika mamlaka zao. “Tumepata uzoefu mzuri katika banda hili kuhusu namna Jiji la Dodoma linavyotangaza fursa za uwekezaji na kutoa huduma kwa wananchi” alisema Mwasongwe.

Kwa upande wake, Afisa Biashara wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Ruth Kingu alisema kuwa maonesho hayo yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kuitangaza halmashauri na kuvutia wawekezaji pamoja na wadau mbalimbali. “Tunawakaribisha wananchi, wafanyabiashara na wawekezaji kutembelea banda letu ili kupata huduma na kufahamu fursa mbalimbali zilizopo ndani ya Jiji la Dodoma" alisema Kingu.

Halmashauri ya Jiji la Dodoma inaendelea kushiriki katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara kwa lengo la kutangaza huduma zake, kuonesha fursa za uwekezaji na kuimarisha ushirikiano na wadau mbalimbali wa maendeleo.







Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga (Mb) , amesema Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) yameonyesha mafanikio makubwa ya sekta ya viwanda na biashara pamoja na fursa zinazotolewa na Serikali kwa vijana na wanawake.

Waziri Kapinga amesema hayo akiwa ameambatana na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Balozi Waziri Salum, alipotembelea maonesho hayo julai 01, 2026 yanayoshirikisha waoneshaji 3,722 kutoka nchi 23 ambayo yatafunguliwa rasmi Julai 3 na Rais wa Msumbiji, Mhe. Daniel Francisco Chapo, akiwa ameambatana na Rais wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Aidha, amewataka Watanzania kutembelea maonesho hayo ili kujifunza kuhusu biashara, viwanda na fursa za kuongeza thamani ya mazao.

Amesema bidhaa nyingi zinazozalishwa na wanawake na vijana zinaonesha matokeo ya uwekezaji wa Serikali kupitia mikopo na programu za uwezeshaji.

Na Munir Shemweta, Dar es Salaam

Serikali imetangaza kuanza kutoa vibali vya ujenzi na kufanya majadiliano na wamiliki wa ardhi na nyumba ambao wapo tayari kushiriki kwenye Mpango wa Uendelezaji Upya eneo la Sinza, huku ikisisitiza kuwa mchakato uliopita umefutwa ili kutoa nafasi ya kuanza upya kwa misingi ya uwazi, ushirikishwaji na kujenga maridhiano.

Kauli hiyo ilitolewa Julai 1, 2026 jijini Dar es Salaam na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt. Leonard Akwilapo, alipokutana na wamiliki wa ardhi na nyumba wa Sinza kwa lengo la kuwafafanulia hatua za utekelezaji wa mpango huo na kusikiliza maoni yao.

Dkt. Akwilapo alisema Serikali imeamua kufungua ukurasa mpya baada ya kubaini kuwa mchakato uliopita uliacha malalamiko kutoka kwa baadhi ya wananchi, hivyo vikao vyote vya awali vimefutwa na sasa mazungumzo yanaanza upya kwa ushirikiano na wananchi.

Alieleza kuwa ukuaji wa miji ni jambo lisiloepukika kutokana na ongezeko la watu na mahitaji ya makazi, hivyo Serikali ina wajibu wa kupanga matumizi ya ardhi kwa kuzingatia mahitaji ya sasa na ya baadaye.

Waziri huyo alisema Sinza ya sasa imebadilika kwa kiwango kikubwa ikilinganishwa na ilivyokuwa miaka ya nyuma, jambo ambalo linahitaji mpango mpya wa maendeleo utakaoendana na hadhi yake kama eneo muhimu la makazi na biashara ndani ya Jiji la Dar es Salaam.

"Kama mwananchi anaona mpango huu haufai, hiyo ni haki yake, lakini ipo siku ataona umuhimu wake. Tusiporatibu maendeleo ya miji, tutakuwa na maeneo yasiyo na mpangilio na yenye miundombinu isiyokidhi mahitaji ya wananchi," alisema.

Dkt. Akwilapo alibainisha kuwa uendelezaji upya wa maeneo ya makazi si jambo geni nchini, kwani maeneo kama Posta, Kariakoo, Upanga, Oysterbay na Masaki yamepitia hatua kama hizo na yameendelea kuwa na thamani kubwa zaidi kutokana na upangaji mzuri wa matumizi ya ardhi.

Waziri huyo aliwataka wananchi kuwa makini na watu wasio waaminifu wanaoweza kutumia mchakato huo kuwahadaa au kuwasambazia taarifa zisizo sahihi kwa manufaa binafsi.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, alisema mafanikio ya mpango huo yatategemea kiwango cha ushirikishwaji wa wananchi na kuzingatia maoni yao.

Alipendekeza muda wa ukusanyaji wa maoni uongezwe kwa miezi mitatu ili wananchi wengi zaidi wapate nafasi ya kuelewa mpango huo na kutoa maoni yao kabla ya hatua za utekelezaji kuanza.

"Wananchi wasikilizwe, maoni yao yazingatiwe na rasimu iboreshwe ili iakisi matakwa yao. Serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan haiwezi kupora haki za wananchi bali itafuata sheria, kanuni na taratibu zote zinazotambuliwa," alisema Profesa Mkumbo.

Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhandisi Anthony Sanga aliwataka wamiliki wa ardhi na nyumba wa Sinza kuwa watulivu na kutochukua maamuzi ya haraka ya kuuza maeneo yao kutokana na taarifa zisizo rasmi.

Alisema thamani ya ardhi katika eneo la Sinza imeongezeka maradufu hivyo wananchi wanapaswa kutambua fursa iliyopo badala ya kufanya maamuzi yatakayowagharimu baadaye.

Akizungumza kwa niaba ya Kamati ya Wamiliki wa Ardhi na Nyumba wa Sinza, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Bw. Asibwene Lumuli, alisema ushirikiano kati ya Serikali na wananchi ndio utakaohakikisha mpango huo unatekelezwa kwa mafanikio na kwa manufaa ya pande zote.Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Leonard Akwilapo akizungumza na wamiliki wa ardhi na Nyumba Sinza wakati wa Kikao kujadili uendelezaji upya eneo la Sinza Dar es Salaam tarehe 1 Julai 2026.Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Leonard Akwilapo akizungumza na baadhi ya wamiliki wa ardhi na Nyumba Sinza mara baada ya Kikao kujadili uendelezaji upya eneo la Sinza Dar es Salaam tarehe 1 Julai 2026.Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhandisi Anthony Sanga akizungumza katika kikao kati ya waziri wa Ardhi na wamiliki wa ardhi na Nyumba Sinza wakati wa Kikao kujadili uendelezaji upya eneo la Sinza Dar es Salaam tarehe 1 Julai 2026.Meya wa Manispaa ya Ubungo Mstahiki Lawrence Mlaki akizungumza wakati wa kikao kati ya waziri wa Ardhi na wamiliki wa ardhi na Nyumba Sinza wakati wa Kikao kujadili uendelezaji upya eneo la Sinza Dar es Salaam tarehe 1 Julai 2026.Mwenyekiti wa Kamati ya wamiliki wa ardhi na Nyumba Sinza Bw. Asibwene Lumuli akizungumza katika kati ya waziri wa Ardhi na wamiliki wa ardhi na Nyumba Sinza wakati wa Kikao kujadili uendelezaji upya eneo la Sinza Dar es Salaam tarehe 1 Julai 2026.Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Leonard Akwilapo akisalimiana na Mkuu wa wilaya ya Ubungo Bw, Albert Msando wakati wa Kikao kujadili uendelezaji upya eneo la Sinza Dar es Salaam tarehe 1 Julai 2026.Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Leonard Akwilapo akiwa katika picha ya pamoja na kamati ya wamiliki wa ardhi na Nyumba Sinza mara baada ya Kikao kujadili uendelezaji upya eneo la Sinza Dar es Salaam tarehe 1 Julai 2026.Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Leonard Akwilapo akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wamiliki wa ardhi na Nyumba Sinza mara baada ya Kikao kujadili uendelezaji upya eneo la Sinza Dar es Salaam tarehe 1 Julai 2026.Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo akizungumza wakati wa Kikao kujadili uendelezaji upya eneo la Sinza Dar es Salaam tarehe 1 Julai 2026. (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)

 

Kufuatia mwaliko wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Daniel Francisco Chapo Rais wa Jamhuri ya Msumbiji, anatarajiwa kuanza ziara ya kikazi ya siku tatu nchini kuanzia tarehe 02 hadi 04 Julai, 2026.

 Wakati wa ziara hiyo, Mheshimiwa Rais Chapo anatarajiwa kufanya mazungumzo rasmi na mwenyeji wake, Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

 Mazungumzo hayo yatajikita katika kuimarisha ushirikiano wa pande mbili katika nyanja mbalimbali zikiwemo biashara, uwekezaji, uchukuzi, nishati pamoja na kuangazia maeneo mapya ya ushirikiano yenye maslahi ya pamoja kwa wananchi wa nchi hizi mbili. 

Mnamo tarehe 03 Julai 2026, Mheshimiwa Rais Chapo anatarajiwa kufungua rasmi Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (DITF), maarufu kama Sabasaba, yatakayowakutanisha wafanyabiashara, wawekezaji na wadau mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi kwa lengo la kukuza biashara, uwekezaji na ushirikiano wa kiuchumi. 

Aidha, Mheshimiwa Rais Chapo atamtembelea Mama Maria Nyerere, Mjane wa Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kwa lengo la kutoa heshima na kutambua mchango wa viongozi waasisi katika kuimarisha uhusiano wa kindugu kati ya Tanzania na Msumbiji, hususan wakati wa harakati za ukombozi wa Bara la Afrika.

 Ziara ya Mheshimiwa Rais Chapo ni kielelezo cha uhusiano imara wa kihistoria na ushirikiano wa karibu kati ya Tanzania na Msumbiji, na inatarajiwa kuendelea kufungua fursa mpya za ushirikiano katika nyanja mbalimbali za maendeleo.

 Itakumbukwa kuwa, ziara hii ni ya tatu kwa Mheshimiwa Rais Chapo nchini Tanzania tangu alipoingia madarakani mwaka 2024, jambo linaloakisi dhamira ya viongozi wa nchi hizi mbili ya kuendelea kuimarisha mahusiano ya kirafiki na ushirikiano wa karibu, yaliyojengwa juu ya historia ya ujirani mwema na mshikamano wa muda mrefu.


NA DENIS MLOWE, IRINGA


MBUNGE wa Jimbo la Isimani, Emanuela Mtatifikolo Kaganda, ametoa msaada wa mabati kwa waendesha bodaboda wa kijiji cha Itunundu kilichoko kata ya Itunundu jimbo la Ismani kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa kijiwe chao cha kusubiri abiria, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono jitihada zao za kuboresha mazingira ya kazi.

Akizungumza kabla ya kukabidhi msaada huo, Mtatifikolo alisema kuwa bodaboda ni kundi muhimu katika kuchochea uchumi na kutoa huduma za usafiri kwa wananchi, hivyo linastahili kupewa ushirikiano na mazingira bora ya kufanyia kazi.

Alieleza kuwa ujenzi wa kijiwe hicho utawasaidia waendesha bodaboda kupata sehemu salama na yenye staha ya kusubiri wateja, sambamba na kuimarisha mpangilio wa shughuli zao.

Mbunge huyo aliwataka wanufaika kuhakikisha wanatumia mabati hayo kwa lengo lililokusudiwa na kukamilisha ujenzi wa kijiwe hicho kwa wakati, huku akisisitiza umuhimu wa kutunza miundombinu hiyo mara baada ya kukamilika.

Kwa upande wao, waendesha bodaboda walimshukuru Mbunge huyo kwa msaada alioutoa, wakisema utachangia kwa kiasi kikubwa kukamilisha ujenzi wa kijiwe hicho na kuboresha mazingira yao ya kazi pamoja na huduma wanazozitoa kwa wananchi.

Walisema kuwa kutokana na joto kali la tarafa ya Pawaga ambapo inapatikana kijiji cha Itunundu msaada huo utasaidia kuepukana na hali hiyo kitu ambacho mbunge amejitoa kwa lengo la kusaidia vijana.





Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali imeelekeza halmashauri zote nchini kutenga asilimia tano ya mapato yao ya ndani kwa ajili ya ujenzi na uboreshaji wa miundombinu ya biashara ili kuwawezesha wananchi, hususan vijana na wanawake, kufanya shughuli za kiuchumi katika mazingira bora na yenye tija.

Akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika Uwanja wa Ingwe Sekondari, Jimbo la Tarime Vijijini, wilayani Tarime, mkoani Mara, leo Jumatano, Julai 1, 2026, Waziri Mkuu alisema hatua hiyo inalenga kuondoa changamoto za maeneo ya biashara na kuongeza fursa za uzalishaji na ajira.

"Tumeenda kuweka asilimia tano kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya maeneo ya biashara. Na kwenye hiyo asilimia tano, nimewaelekeza wenzetu wa TAMISEMI kwamba kama kuna eneo vijana wanalitaka kwa ajili ya kufanyia biashara, hata kama hilo eneo lina wamiliki, tumieni asilimia tano kulinunua. Msiwapeleke vijana kufanyia biashara maeneo ya mbali ambayo hayaendani na biashara wanazozifanya."

Aidha, Waziri Mkuu alisema Serikali imepitisha utaratibu wa kuwapa wafanyabiashara wanaoanzisha biashara mpya kipindi cha mwaka mmoja kabla ya kuanza kulipa kodi, ili kuwapa nafasi ya kuimarisha biashara zao.

"Wale vijana na kina mama wanaoanzisha biashara mpya hawataanza kudaiwa kodi mara wanapoanzisha biashara. Sasa watakuwa na likizo ya mwaka mzima ili wajipange katika kuimarisha biashara zao."

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu alisema Serikali itawasilisha bungeni marekebisho ya sheria inayohusu kutaifisha mifugo kwa lengo la kuondoa adhabu ambazo zimekuwa zikiwaathiri wafugaji bila kuathiri juhudi za uhifadhi.

"Bunge lijalo la mwezi wa nane tunaenda kufuta sheria inayotaifisha mifugo ya Watanzania. Tumetathmini tukagundua kwamba sheria hiyo inawatia umaskini Watanzania. Tumegundua katika baadhi ya maeneo adhabu imekuwa kubwa kuliko kosa lililotendwa."

Pia, Waziri Mkuu alisema Serikali imeelekeza kusitishwa kwa utaratibu wa kukamata vitendea kazi vya wananchi kwa madai ya faini, akisema hatua hiyo imekuwa ikikwamisha shughuli za uzalishaji na kujiongezea kipato.

"Kama mtu anadaiwa faini, mwacheni kitendea kazi chake, aendelee kufanya kazi ili awalipe faini. Tuache utekelezaji wa sheria wa kishamba shamba."

Sambamba na hayo, Waziri Mkuu alisisitiza kuwa Serikali haitavumilia ubadhirifu na matumizi mabaya ya madaraka katika utumishi wa umma.

"Mtu akiiba, mtumishi wa umma akiiba, msimhamishe. Mfukuzeni kazi. Hatuna uhaba wa watu wa kufanya kazi."

Akihitimisha, Waziri Mkuu aliwataka wananchi kuendelea kulinda amani, umoja na usalama wa nchi, akisisitiza kuwa maendeleo ya taifa na ustawi wa wananchi unategemea kuwepo kwa mazingira ya amani, utulivu na mshikamano.






Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imewasihi wadau wa ununuzi wa umma na wananchi kwa ujumla kutembelea banda la Mamlaka ya Rufani kupata uelewa juu ya majukumu na huduma mbalimbali zinazotolewa na taasisi hiyo hususan matumizi ya Moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST.


Wito huo umetolewa na Mkuu wa Sehemu ya Huduma za Sheria PPAA, Bi. Agnes Sayi kwa niaba ya Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando. Bi Sayi alitoa wito huo leo tarehe 01 Julai, 2026 katika Banda la Wizara ya Fedha Jijini Dar es Salaam kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba). 

Pamoja na mambo mengine, PPAA katika maonesho hayo inatoa elimu kuhusu uamuzi juu ya rufaa zinazotokana na mchakato wa ununuzi wa umma, uamuzi juu ya rufaa zinazotokana na kufungiwa kushiriki katika michakato ya ununuzi wa umma pamoja na uamuzi juu ya malalamiko yanayotokana na kushindwa kwa Afisa Masuuli kutoa uamuzi ndani ya muda uliowekwa.

“Maeneo mengine yanayotolewa elimu ni uamuzi juu ya malalamiko baada ya mkataba wa ununuzi kuanza kutekelezwa, uamuzi juu ya maombi ya kuongezewa muda wa kuwasilisha rufaa nje ya muda uliowekwa, uamuzi juu ya maombi ya utekelezaji wa amri ya Mamlaka ya Rufani, uamuzi juu ya maombi ya kufuta uamuzi uliotolewa bila kusikiliza upande mwingine (Ex Parte decision) na uamuzi juu ya maombi ya kurejesha rufaa,” amesema Bi. Sayi

Maonesho hayo yameanza tarehe 28 Juni yataendelea hadi 13 Julai 2026 katika Viwanja vya Mwl. Nyerere Jijini Dar es Salaam. Aidha, Taasisi mbalimbali za Umma zimeshiriki maonesho hayo kwa lengo la kuonesha huduma wanazotoa kwa wananchi kwa kaulimbiu: Maonesho ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba, Fahari ya Tanzania.




 

 

Naibu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya EWURA, Mha. Ngosi Mwihava (kushoto) na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Ndg. Gerald Maganga (Kulia) wakimkabidhi Mh. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan mfano wa hundi kama ishara ya kukabidhi Hazina mchango wa kisheria wa taasisi hiyo wa Sh. 10.6 bilioni, kwa mwaka wa Fedha 2025/26, kwenye hafla iliyofanyika Ikulu jana.

 
Na FARIDA MANGUBE MOROGOGO


Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima, amesema kada ya Maendeleo ya Jamii inapaswa kuwa injini ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwa kuongoza mageuzi ya fikra, kuimarisha uchumi wa wananchi na kujenga jamii yenye maarifa, uzalishaji, ubunifu na uzalendo.

Ameyasema hayo Leo Julai 1 Mjini Morogoro wakati akifungua kikao kazi cha Wakuu wa Vitengo vya Maendeleo ya Jamii ngazi ya mikoa, Dkt. Gwajima amesema mafanikio ya Dira ya 2050 hayatategemea ukubwa wa bajeti au idadi ya miradi ya maendeleo, bali uwezo wa kubadilisha fikra na tabia za Watanzania katika kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya Taifa.

Waziri Gwajima amewataka wakuu wa vitengo vya maendeleo ya jamii kuhamasisha mapinduzi ya fikra yatakayojenga utamaduni wa kuthamini kazi, uzalishaji, ubunifu, matumizi ya teknolojia, uwajibikaji na kujitegemea. Aidha, alisema ni wakati wa kuifanya taaluma ya maendeleo ya jamii itumie mifumo ya kidijitali na taarifa zinazotokana na ushahidi ili kupanga na kutekeleza afua zenye matokeo yanayopimika kwa wananchi.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Eliakim Maswi, amesema utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 unahitaji mabadiliko makubwa katika sekta ya maendeleo ya jamii ili iweze kutekeleza wajibu wake kwa ufanisi.

Ameeleza kuwa pamoja na Serikali kuendelea kuwekeza katika miradi mikubwa ya maendeleo, mafanikio yake yatategemea pia mabadiliko ya wananchi kupitia kazi ya maafisa wa maendeleo ya jamii.

Naye Mwenyekiti wa Wakuu wa Vitengo vya Maendeleo ya Jamii Tanzania Bara, Elis Simonile, amesema kikao hicho kimewapa fursa ya kujitathmini, kubaini changamoto na vikwazo vinavyoikabili kada hiyo pamoja na kuweka mikakati ya kuboresha utendaji kwa lengo la kuleta mabadiliko ya tabia na kuimarisha uzalendo miongoni mwa wananchi.

Simonile amesema vitendea kazi walivyokabidhiwa vitasaidia kuongeza ufanisi wa kazi kwa kuwa awali uhaba wa vifaa ulikuwa kikwazo kikubwa katika kuwafikia wananchi. Aliongeza kuwa matumizi ya mifumo ya kidijitali yatawezesha ukusanyaji na uchambuzi wa taarifa sahihi, hivyo kurahisisha utoaji wa ujumbe na utekelezaji wa afua za maendeleo ya jamii kwa ufanisi zaidi.

Kikao kazi hicho kilichowakutanisha Wakuu wa Vitengo vya Maendeleo ya Jamii kutoka mikoa yote ya Tanzania Bara kililenga kutathmini utekelezaji wa majukumu ya kada hiyo, kubadilishana uzoefu na kuweka mikakati ya kuimarisha mchango wake katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Kikao hicho kilihitimishwa kwa ugawaji wa vitendea kazi, ikiwemo kompyuta mpakato kwa lengo la kuimarisha matumizi ya mifumo ya kidijitali katika ukusanyaji, uchambuzi na utoaji wa taarifa za maendeleo ya jamii kwa wakati.







Standard Chartered Tanzania kwa kushirikiana na Nipe Fagio imeadhimisha miaka 20 ya programu ya kujitolea kwa jamii ya Standard Chartered duniani kwa kufanya zoezi la kila mwaka la usafi wa fukwe katika Ufukwe wa Silversand, Kunduchi.

Jumla ya washiriki 74, wakiwemo watoto 20, walishiriki katika zoezi hilo lililolenga kuchangia uhifadhi wa mazingira na kuhamasisha ushiriki wa wafanyakazi katika shughuli za maendeleo ya jamii.

Akizungumza kuhusu shughuli hiyo, Afisa Mtendaji Mkuu na Mkuu wa Kitengo cha Coverage wa Standard Chartered Bank Tanzania, Geofrey Mchangila, alisema:

"Zoezi la mwaka huu lina umuhimu wa pekee kwetu kwani linafanyika wakati Standard Chartered inaadhimisha miaka 20 ya kujitolea kwa jamii duniani kote. Tunaamini kuwa mabadiliko ya kweli huanza pale watu wanapounganisha nguvu zao. 

Kupitia ushirikiano wetu na wafanyakazi, familia zao pamoja na Nipe Fagio, tunaendelea kuchangia kulinda ukanda wa pwani wa Tanzania na kujenga jamii zenye afya bora na mazingira endelevu kwa vizazi vijavyo."

Katika zoezi hilo, washiriki walisafisha eneo lenye ukubwa wa takribani mita za mraba 4,000 za ufukwe na kukusanya kilo 506 za taka zilizohifadhiwa katika mifuko 55. 

Uchambuzi wa taka zilizokusanywa ulionyesha kuwa plastiki, hususan povu la polystyrene na chupa za plastiki za vinywaji, ndizo zilikuwa taka zilizopatikana kwa wingi, hali inayodhihirisha umuhimu wa kuendelea kuchukua hatua za kudhibiti uchafuzi wa mazingira ya bahari.

Kwa kipindi cha miaka mitatu iliyopita, kupitia ushirikiano wake na Nipe Fagio, Standard Chartered Tanzania imefanikisha jumla ya kampeni tano za usafi wa fukwe, ikihusisha washiriki 594, kusafisha zaidi ya mita za mraba 32,000 za ukanda wa pwani na kukusanya karibu tani tano za taka.

Mpango huu ni sehemu ya mkakati mpana wa Standard Chartered wa kuendeleza uhimilivu wa mazingira na maendeleo endelevu, huku ukiunga mkono Malengo ya Maendeleo Endelevu ya Umoja wa Mataifa (SDGs), hususan Lengo la 13 la Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi, Lengo la 14 la Kuhifadhi Maisha ya Chini ya Maji na Lengo la 17 la Kuimarisha Ushirikiano kwa Ajili ya Kufanikisha Malengo.

Standard Chartered inapoendelea kuadhimisha miaka 20 ya programu yake ya kujitolea kwa jamii, inaendelea kuwahamasisha wafanyakazi wake kutumia muda, ujuzi na utaalamu wao kuleta mabadiliko chanya na endelevu katika jamii na mazingira.










Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi Mteule wa Tanzania nchini Uganda, Mhe. Balozi Meja. Jen. Marco Elisha Gaguti, mazungumzo yaliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam leo tarehe 01 Julai 2026.

Mazungumzo hayo ni kufuatia, Mhe. Balozi Gaguti, kufika kwa Makamu wa Rais kwa lengo la kumuaga akielekea katika Kituo chake cha kazi nchini Uganda, mara baada ya kuteuliwa hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.









Top News