Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Kagera Mhe. Erasto Sima ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Bukoba, amesema Serikali itaendelea kuwawezesha vijana kiuchumi kupitia Sekta ya Uvuvi ili kukabiliana na changamoto ya ajira nchini.

Mhe. Sima  amesema hayo Mei 9, 2026 katika hafla ya kukabidhi mitaji kwa njia ya mikopo yenye masharti nafuu kwa vijana 47 walionufaika na Programu ya Jenga Kesho Iliyobora (BBT–Uvuvi) iliyofanyika Katika Mwalo wa Bilolo Kemondo  Bukoba. 

“Programu hii inalenga kutoa mafunzo kwa vitendo pamoja na mitaji ili kuwawezesha vijana kujiajiri na kuwa wawekezaji katika Sekta ya Uvuvi,” amesema Mhe. Sima

Aidha, Mhe. Sima amesema kuwa hafla hiyo ni mwendelezo wa ugawaji wa mitaji uliozinduliwa Machi 7, 2026 katika eneo la FETA Nyegezi mkoani Mwanza, ambapo vijana 55 walikabidhiwa pembejeo mbalimbali za ufugaji wa samaki kwa vizimba.

Mhe. Sima amewataka wanufaika hao kutumia fursa waliyopewa kwa uwajibikaji, nidhamu na uadilifu ili kuhakikisha miradi hiyo inaleta matokeo chanya kwao binafsi na Taifa kwa ujumla.

Naye Mwakilishi wa Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Imelda Adam ambaye ni Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Utafiti na Mafunzo amesema Serikali kupitia Programu ya Building a Better Tomorrow ( BBT) ni utekelezaji wa dhamira ya awamu ya sita chini ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ikiwa na lengo la  kuwajengea vijana uwezo wa kushiriki Katika shughuli za uzalishaji mali kupitia Sekta ya uvuvi na ufugaji wa samaki.

Kwa upande wake mwakilishi wa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Elimu na Mafunzo ya Uvuvi (FETA) Bi. Merisia Mparazo amesema kupitia programu ya BBT-Uvuvi, Serikali inaendelea kuwawezesha vijana kushiriki kikamilifu Katika shughuli za uzalishaji mali kupitia ufugaji wa samaki Kwa kutumia teknolojia ya vizimba, pia FETA imepewa jukumu la kusimamia utekelezaji wa mradi huo Katika Kanda ya Ziwa ikiwemo uratibu wa vijana, usambazaji wa vifaranga bora vya samaki, vifaa muhimu pamoja na chakula cha samaki ili kuhakikisha uzalishaji wenye tija na ubora unaotarajiwa.




 

 

 


📌 Utawezesha Mkoa wote Kagera kuunganishwa na Gridi ya Taifa

📌 Zaidi ya Bilioni 270 kutumika kutekeleza mradi
📌 Mradi kukamilika ndani ya miezi 24

Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi leo Mei 9, 2026 ameweka jiwe la msingi la mradi wa njia ya kusafirisha umeme wa KV 220 Benaco–Kyaka pamoja na Kituo cha Kupoza Umeme cha Benaco wilayani Ngara, mkoani Kagera.

''Tunatarajia ndani ya miezi 24 Mkoa wa Kagera uwe umeunganishwa katika Gridi ya Taifa na changamoto za umeme ziwe historia,” alisema Mhe. Ndejembi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Ngara, Bw. Mathias Kahabi, akimwakilisha Mkuu wa Mkoa amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Waziri wa Nishati kwa kuendelea kuwekeza katika miradi ya maendeleo ya umeme wilayani humo.

Amesema katika Jimbo la Ngara vijiji vyote 75 tayari vimefikiwa na huduma ya umeme, huku vitongoji 219 kati ya vitongoji 389 vikiwa tayari vimeunganishiwa umeme.

Akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi huo Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange amesema mradi huo utaongeza uhakika wa upatikanaji wa umeme na kuchochea shughuli za kiuchumi Mkoa wa Kagera.

 “TANESCO imejipanga kuhakikisha mradi huu unakamilika kwa wakati na kwa viwango vinavyotakiwa,” alisema Bw. Twange.

Naye Mjumbe wa Bodi ya TANESCO, Bi. Zuhura Bundala amesema mradi huo utafungua fursa za maendeleo, ajira kwa vijana na kuongeza uzalishaji mali kwa wananchi wa Kagera.

 “Mradi huu utafungua fursa nyingi za maendeleo kwa wananchi wa Kagera,” alimalizia Bi. Bundala.

Katika hatua nyingine Waziri Ndejembi ameuagiza uongozi wa TANESCO kuhakikisha wananchi hawaendelei kusubiri huduma ya umeme kwa muda mrefu kwa kutafuta transfoma kubwa zitakazosaidia kuongeza upatikanaji wa umeme wakati utekelezaji wa mradi ukiendelea.

Sambamba na hilo, amewataka wakandarasi kuhakikisha wanakamilisha mradi huo kwa wakati bila ucheleweshaji, huku akisisitiza umuhimu wa kutoa ajira kwa wananchi wa maeneo husika pamoja na kulipa fidia stahiki kwa waliopisha utekelezaji wa mradi.

“Niwatake wakandarasi kukamilisha mradi huu kwa wakati bila ucheleweshaji wowote. Vilevile, hakikisheni wananchi wanapata ajira kupitia utekelezaji wa mradi huu pamoja na kulipwa fidia zao kwa wakati,” amesema Ndejembi.

Mkoa wa Kagera mpaka sasa umefanikiwa kwa wilaya mbili pekee za Biharamulo na Ngara kuunganishwa kwenye Gridi ya Taifa kukamilika kwa mradi huo kutawezesha Mkoa wote kuungwa kwenye Gridi ya Taifa






*China yafungua mlango wa ushuru sifuri kwa bidhaa za Tanzania

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
SERIKALI imesema itaendelea kuwawezesha wafanyabiashara wa Tanzania wanaosafirisha bidhaa nje ya nchi ili wanufaike kikamilifu na fursa za masoko ya kimataifa na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, wakati wa mkutano wa wadau kuhusu matumizi ya fursa ya kuuza bidhaa nchini China bila ushuru, uliofanyika jijini Dar es Salaam.

Kapinga amesema mkutano huo ni muhimu kwa kuwa unalenga kuwaunganisha wasafirishaji wa bidhaa kwenda China na kuweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha bidhaa za Tanzania zinafikia masoko ya kimataifa kwa ushindani mkubwa.

Amesema serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan imejipanga kuwawezesha wafanyabiashara katika kila hatua ili kutimiza azma ya kukuza diplomasia ya uchumi na kuongeza mchango wa sekta binafsi katika maendeleo ya taifa.

“Tunachojadili hapa kisiwekwe kabatini. Wafanyabiashara wanahitaji kutatuliwa changamoto zao ili waweze kutumia fursa zilizopo,” amesema Kapinga.

Aidha, amesema mfanyabiashara hapaswi kuambiwa hana vigezo vya kushiriki soko la kimataifa, bali juhudi zinapaswa kuelekezwa katika kumwezesha kufikia viwango vinavyotakiwa kwa biashara hizo.

Kapinga ameihimiza sekta binafsi kujipanga kutumia soko la China, akieleza kuwa mazingira yaliyowekwa ya kuingiza bidhaa bila ushuru yanafungua fursa kubwa kwa wazalishaji na wasafirishaji wa Tanzania.

Amesema serikali itaendelea kuboresha mazingira ya biashara kwa kuwekeza katika ubora wa bidhaa, kuongeza thamani ya mazao, kuimarisha usindikaji na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Kwa mujibu wa Kapinga, kupitia mifumo mbalimbali ya biashara ya upendeleo, bidhaa nyingi zinazozalishwa Tanzania zinaweza kuingia katika masoko makubwa duniani bila ushuru au kwa masharti nafuu ya ushuru, jambo linaloongeza ushindani wake katika soko la dunia.

Hata hivyo, amewataka wafanyabiashara kuzingatia kanuni za asili ya bidhaa kwa kuhakikisha bidhaa zinazouzwa nje zimezalishwa nchini au zimeongezewa thamani kwa kiwango kinachokubalika kimataifa.

Kwa upande wake, Balozi wa China nchini Tanzania amesema hamasa iliyooneshwa na washiriki wa mkutano huo inaashiria nia kubwa ya wafanyabiashara kutumia fursa hiyo, japokuwa bado kuna changamoto ya uelewa wa sera na namna bora ya kuitumia kwa vitendo.

Amesema China itaendelea kushikilia sera ya urafiki, uaminifu na ushirikiano wa dhati kwa kutumia mpango wa ushuru wa sifuri kama nyenzo ya kuimarisha biashara na maendeleo ya pamoja kati ya China, Tanzania na Afrika kwa ujumla.

Aidha, amesema Serikali ya China imeanza utekelezaji wa sera ya ushuru wa sifuri kwa nchi 20 za Afrika zenye uhusiano wa kidiplomasia na China ambazo hazipo katika kundi la nchi maskini zaidi duniani, huku mpango huo ukitarajiwa kudumu kwa miaka miwili.

Naye Mshauri wa Rais wa Masuala ya Kilimo, Geoffrey Kirenga, amesema Tanzania ina nafasi kubwa ya kunufaika na soko hilo kutokana na uzalishaji wa bidhaa bora zikiwemo korosho, kahawa na viungo.

Kirenga amesema tayari uwekezaji katika viwanda vya kuongeza thamani unaendelea, sambamba na ununuzi wa mashine za kisasa kutoka China, hatua inayolenga kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania kabla ya kusafirishwa nje ya nchi.

Katika hatua nyingine, Kapinga ameagiza TanTrade kuweka mikakati endelevu ya kuwawezesha wafanyabiashara ili Tanzania iwe kitovu cha biashara ya kimataifa na uzalishaji wa viwanda wenye ushindani katika ukanda wa Afrika Mashariki.






*Uwezo wa Bandari ya Dar kuongezeka maradufu ifikapo 2030

Na Mwandishi Wetu
SHIRIKA la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) limeanza mikakati ya kupunguza msongamano wa makasha katika Bandari ya Dar es Salaam kwa kuongeza ufanisi wa Bandari Kavu nchini.

Hayo yalisemwa na Mkurugenzi Mkuu wa TASAC, Mohamed Salum, wakati wa kikao cha wadau wa mamlaka mbalimbali za Serikali kilichofanyika jijini Dar es Salaam.

Salum alisema lengo la kikao hicho ni kujadili namna ya kuanzisha na kuendeleza bandari kavu kwa kufuata taratibu na sheria, pamoja na kutafuta suluhisho la changamoto ya foleni ya magari katika jiji hilo.

Alieleza kuwa changamoto zilizopo ni pamoja na msongamano wa magari barabarani, ucheleweshaji wa upatikanaji wa mizigo kwa wateja, kuongezeka kwa gharama za usafirishaji, pamoja na uwezo mdogo wa baadhi ya bandari kavu kushindwa kuhudumia mizigo mingi.

Kwa mujibu wa TASAC, Bandari ya Dar es Salaam inapokea wastani wa makontena 110,000 kwa mwezi, ambapo asilimia 45 ya makontena hayo husafirishwa kwenda nchi jirani zinazotumia bandari hiyo ikiwemo Zambia, Malawi,Jamhuri ya Demokrasia ya Congo (DRC) , Rwanda pamoja na Burundi.

Alisema uwezo wa sasa wa Bandari ya Dar es Salaam ni kuhudumia makontena 28,000 kwa wakati mmoja, huku kitaalamu kiwango cha matumizi kisichopaswa kuzidi asilimia 65 ili kuhakikisha ufanisi wa huduma unaendelea kuwa mzuri.

“Bandari si sehemu ya kuhifadhi makontena bali ni eneo la kupokelea na kusafirisha mizigo. Ndiyo maana uwepo wa bandari kavu ni muhimu katika kusaidia shughuli hizo,” alisema Salum.

Aidha, alisema uwezo wa bandari kavu zilizopo kwa sasa jijini Dar es Salaam hauwezi kuhifadhi zaidi ya makontena 37,000, hali inayosababisha changamoto kubwa kutokana na ongezeko la mizigo inayoingia na kutoka nchini.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Udhibiti na Usimamizi wa Huduma za Usafiri Majini, Nelson Mlali, alisema zaidi ya asilimia 80 ya bandari kavu nchini zipo Dar es Salaam kutokana na mahitaji makubwa ya soko na uwepo wa viwanda vingi.

Mlali alisema Wilaya ya Temeke inaongoza kwa kuwa na bandari kavu 74 sawa na asilimia 64.3, ikifuatiwa na Ilala yenye bandari kavu 22, Kigamboni bandari kavu 13, Kinondoni nne na Ubungo mbili.

Naye Mkurugenzi Msaidizi wa Usafiri wa Majini kutoka Wizara ya Uchukuzi, Mussa Shashula, alisema Serikali inaendelea kuwekeza katika miundombinu ya bandari kavu ili kuongeza ufanisi wa Bandari ya Dar es Salaam.

Alisema matokeo ya uwekezaji huo yameanza kuonekana baada ya kiwango cha mizigo bandarini kuongezeka kutoka tani milioni 18 mwaka 2021/22 hadi tani milioni 32 mwaka 2024/25.

 

 


Na Janeth Raphael MichuziTv

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ameliagiza Jeshi la Magereza kufanya tafiti za kina zitakazowezesha kuanzishwa kwa mfuko maalumu wa kuwasaidia wafungwa wenye ujuzi wanaporejea uraiani, ili waweze kujitegemea kiuchumi na kuepuka kurejea katika makosa ya uhalifu.

Rais Samia amesema hatua hiyo ni sehemu ya kuimarisha mfumo wa urekebishaji nchini kwa kuhakikisha wafungwa wanaopata mafunzo ya ufundi na stadi mbalimbali wakiwa magerezani wanapata mazingira rafiki ya kuanza maisha mapya baada ya kutumikia vifungo vyao.

Ametoa maelekezo hayo leo Mei 9, 2026, wakati akihutubia hafla ya kuhitimisha Mafunzo ya Uongozi Ngazi ya Juu Kozi Na. 28 pamoja na Uongozi Daraja la Pili Kozi Na. 48 iliyofanyika katika Chuo cha Taaluma ya Urekebishaji Tanzania (TCTA), Ukonga jijini Dar es Salaam.

Katika hotuba yake, Rais Samia alisema wafungwa wengi wamekuwa wakipata ujuzi muhimu wakiwa magerezani kupitia mafunzo mbalimbali ya ufundi stadi, ushonaji, kilimo, useremala na shughuli nyingine za uzalishaji, lakini changamoto kubwa imekuwa ni ukosefu wa mtaji au mifumo ya kuwawezesha kuanza maisha mapya wanapotoka gerezani.

Amesema kuanzishwa kwa mfuko huo kutasaidia kuwapa nguvu ya kuanza upya kwa kutumia maarifa na taaluma walizozipata, jambo litakalosaidia kupunguza matukio ya kurudia makosa pamoja na kuongeza mchango wao katika maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.

“Tunapaswa kuwapa nafasi ya pili ya maisha. Kama wamejifunza kazi na stadi mbalimbali wakiwa magerezani, basi wanapotoka wanahitaji kuungwa mkono ili waweze kujitegemea na kuwa sehemu ya maendeleo ya nchi,” alisisitiza Rais Samia.

Aidha, amemuelekeza Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza Tanzania, Jeremiah Katungu kushirikiana na wadau mbalimbali kufanya tafiti za sera na mifumo bora itakayowezesha utekelezaji wa mpango huo kwa ufanisi.

Rais Samia pia alipongeza Jeshi la Magereza kwa kuendelea kuboresha mfumo wa urekebishaji wa wafungwa kwa kuwapatia elimu, maadili na stadi za maisha zinazowaandaa kuwa raia wema baada ya kumaliza vifungo vyao.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali, maafisa wa Jeshi la Magereza pamoja na washiriki wa mafunzo waliohitimu kozi hizo za uongozi.































 

 

Na Janeth Raphael MichuziTv 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amesisitiza umuhimu wa kulinda na kuheshimu utu, haki na heshima za wafungwa wanawake, akieleza kuwa licha ya makosa yao ya kisheria, bado wanabaki kuwa binadamu wanaostahili kutendewa kwa staha na kuzingatiwa haki zao msingi.
Rais Samia ametoa kauli hiyo leo Jumamosi, Mei 9, 2026, wakati akihutubia katika hafla ya kufunga Mafunzo ya Uongozi Ngazi ya Juu Kozi Na. 48 ya mwaka wa masomo 2025/26, iliyofanyika katika Chuo cha Taaluma ya Urekebishaji Tanzania (TCT), Ukonga jijini Dar es Salaam.

Katika hotuba yake, Rais Samia amesisitiza kuwa wafungwa wanawake wana mahitaji maalum kutokana na maumbile yao na majukumu yao ya kibinadamu, hivyo ni muhimu kwa watendaji wa taasisi za marekebisho kuzingatia tofauti hizo katika utoaji wa huduma na usimamizi wa magereza.

“Wale mnaowasimamia wafungwa wanawake, naomba mhakikishe haki zao, utu wao na heshima yao vinazingatiwa. Ni kweli wamekosea na wanaadhibiwa, lakini bado ni binadamu wenye stahiki zao,” amesema Rais Samia.

Aidha, ameeleza kuwa taasisi za marekebisho zinapaswa kuwa sehemu ya kujenga na kurekebisha tabia za wafungwa badala ya kuwa sehemu ya kuvunja matumaini yao. Amesisitiza umuhimu wa uongozi unaozingatia misingi ya utu, usawa na uadilifu katika usimamizi wa magereza.

Rais Samia pia amehimiza kuimarishwa kwa mifumo ya malezi na mafunzo ndani ya magereza ili kuwawezesha wafungwa kupata ujuzi utakaowasaidia pindi watakapomaliza vifungo vyao, na kurejea katika jamii wakiwa na uwezo wa kujitegemea na kuchangia maendeleo ya taifa.

Kauli hiyo imeendelea kuonesha msisitizo wa Serikali katika kuboresha mfumo wa urekebishaji na kuhakikisha magereza yanakuwa sehemu ya mageuzi chanya ya kijamii badala ya adhabu pekee.







































 


Top News