Na Mwandishi Wetu

Tasnia ya filamu nchini imepata pigo kufuatia kifo cha msanii mkongwe, Mzee Kambi, kilichotokea leo Aprili 27, 2026.

Taarifa za kifo hicho zimethibitishwa na Msemaji wa Shirikisho la Filamu Tanzania, Coletha Raymond, aliyesema kuwa msanii huyo alifariki dunia ghafla alipokuwa akiendelea na shughuli zake za kazi.

Akizungumza kuhusu tukio hilo, Coletha alisema Mzee Kambi alikuwa ametoka mkoani Tabora kikazi na aliporejea alielekea moja kwa moja katika shughuli zake kwenye studio za Pilipili, kabla ya kuanza kujisikia vibaya.

“Ni kweli tumempoteza Mzee Kambi. Alikuwa ametoka Tabora na alipofika alienda moja kwa moja kazini katika studio za Pilipilibl. Akiwa kazini ndipo alipozidiwa ghafla na kukimbizwa hospitali, lakini kwa bahati mbaya alifariki dunia,” alisema Coletha.

Aliongeza kuwa chanzo cha kifo kinahusishwa na matatizo ya kiafya yaliyokuwa yakimsumbua, ikiwemo presha na kisukari.

Aidha, alisema Shirikisho la Filamu Tanzania linaendelea na taratibu za ndani kwa kushirikiana na familia ya marehemu ili kupanga mipango ya mazishi, ambapo taarifa zaidi zitatolewa baadaye.

Kifo cha Mzee Kambi kimeacha pengo kubwa katika tasnia ya filamu nchini, ambapo amekuwa mmoja wa wasanii waliotoa mchango mkubwa katika kukuza sanaa hiyo kwa muda mrefu. 
Na MWANDISHI WETU,

Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) umeendelea kuimarika kwa kasi, ukifikia thamani ya shilingi trilioni 11.2 hadi Machi 2026 kutoka trilioni 4.3 mwaka 2020, hatua inayoakisi ukuaji wa uwekezaji, uimara wa usimamizi na kuongezeka kwa ushiriki wa wananchi kupitia Hifadhi Skimu.

Ukuaji huo umeambatana na upanuzi wa huduma za hifadhi ya jamii, hususan kupitia hifadhi skimu zinazolenga kuwafikia wananchi waliojiajiri, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuongeza wigo wa wanachama na kuimarisha ushirikishwaji wa makundi mbalimbali ya jamii katika mfumo wa hifadhi ya jamii.

Akizungumza jijini Dodoma tarehe 27 Aprili 2026 wakati akifungua Mkutano wa 56 wa Baraza Kuu la Wafanyakazi wa NSSF, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Mhe. Deus Sangu, alisema mafanikio ya Mfuko yanatokana na mageuzi ya usimamizi, uwekezaji wenye tija na matumizi ya teknolojia katika utoaji wa huduma.

Alisisitiza kuwa hifadhi skimu ni nguzo muhimu ya mustakabali wa hifadhi ya jamii nchini, akibainisha kuwa Serikali inalenga kuhakikisha Watanzania wengi zaidi, hususan waliojiajiri, wanajumuishwa katika mfumo huo.

“Upanuzi wa hifadhi skimu ni hatua muhimu ya kuhakikisha hakuna Mtanzania anayebaki nje ya mfumo wa hifadhi ya jamii,” alisema Mhe. Sangu.

Waziri huyo pia aliipongeza NSSF kwa mchango wake katika uchumi wa taifa kupitia uwekezaji katika miradi mbalimbali ya maendeleo inayozalisha ajira na kuchochea ukuaji wa sekta binafsi, akitaja kiwanda cha sukari cha Mkulazi kuwa mfano wa uwekezaji wenye tija.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Bw. Masha Mshomba, alisema mafanikio hayo yametokana na usimamizi madhubuti wa fedha, uwekezaji salama na matumizi ya mifumo ya TEHAMA iliyofikia takribani asilimia 99 ya huduma.

Alisema katika Mpango Mkakati wa miaka mitano (2026/27–2030/31), NSSF inalenga kufikia thamani ya shilingi trilioni 24.7 ifikapo Juni 2031, pamoja na kuongeza wanachama hadi milioni 6.6, huku mkazo ukiwekwa katika kuimarisha mpango wa Hifadhi Skimu na kuzingatia misingi ya mazingira, jamii na utawala bora (ESG). Katika kupata hati safi za ukaguzi kutoka Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), mafanikio hayo yametokana pia na Mfuko kufuata misingi ya utawala bora, uwazi, uwajibikaji na uwekezaji wenye tija, hali inayoendelea kuimarisha imani ya wadau na umma kwa ujumla.

Pamoja na mafanikio hayo, Mfuko unaendelea kukabiliana na changamoto mbalimbali ikiwemo baadhi ya waajiri kutowasilisha michango kwa wakati, kuwasilisha michango chini ya kiwango halisi, pamoja na uelewa mdogo wa masuala ya hifadhi ya jamii kwa baadhi ya makundi ya wananchi, hali inayopatiwa ufumbuzi kupitia elimu na uhamasishaji unaoendelea.

Katika hatua nyingine, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF ametoa pongezi kwa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, akibainisha kuwa Serikali ya Awamu ya Sita imeweka mazingira bora na wezeshi ya ufanyaji kazi, uwekezaji pamoja na biashara, jambo lililochochea ongezeko la wanachama na uimara wa mifumo ya hifadhi ya jamii.

Katika hatua nyingine, Waziri Sangu alieleza kuwa mipango ya Mfuko inaendana kikamilifu na mipango mikuu ya Serikali ikiwemo Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 na Sera ya Taifa ya Kinga ya Jamii. Alisema Serikali inalenga kuhakikisha ifikapo mwaka 2050, takribani asilimia 70 ya Watanzania watakuwa wamefikiwa na mifumo ya hifadhi ya jamii kupitia upanuzi wa Hifadhi Skimu na mifumo jumuishi ya kinga ya kijamii.

Waziri huyo alisema mafanikio ya sekta hiyo ni sehemu ya mwelekeo mpana wa taifa wa kujenga uchumi shirikishi unaomlinda kila Mtanzania.

Mkutano huo wa 56 wa Baraza Kuu la Wafanyakazi wa NSSF unajadili Mpango Mkakati wa Nane pamoja na bajeti ya mwaka wa fedha 2026/27, likiwa ni jukwaa muhimu la kuweka mwelekeo wa baadaye wa Mfuko na mustakabali wa hifadhi ya jamii nchini.


















Na Mwandishi Wetu,Michuzi TV.

MKURUGENZI Mtendaji wa Taasisi ya UONGOZI Kadari Singo amesema kwamba madini ni muhimu si tu kwa rasilimali za kiuchumi bali pia ni nyenzo ya kuleta mabadiliko ya kweli katika maendeleo ya Afrika. 

Hivyo ametoa mwito kwa nchi za Afrika kushirikiana, kuweka sera madhubuti, na kuwekeza katika sekta ya madini ili kuhakikisha manufaa yake yanawafikia wananchi wote.

Singo ameyasema hayo leo  Aprili 27, 2026, jijini Addis Ababa nchini Ethiopia wakati wa mkutano wa Jukwaa la Kikanda lililoandaliwa na Tume ya Uchumi ya Umoja wa Mataifa kwa Afrika kwa kushirikiana na Taasisi ya UONGOZI.

Kauli mbiu katika jukwaa hilo inasema  “Kuchangamkia Madini Muhimu ya Afrika kwa Ajili ya Ujenzi wa Viwanda Kijani na Maendeleo Endelevu.” 

Singo katika hutuba yake iliyoangazia nafasi ya Afrika katika mustakabali wa uchumi wa dunia unaozingatia nishati safi, amesisitiza nchi za Afrika zinapaswa kushirikiana, kuweka sera madhubuti na kuwekeza katika sekta ya madini ili manufaa yake yanawafikia wananchi wote

“Jukwaa hili limeweka msingi muhimu wa mijadala itakayochochea hatua za vitendo, huku likisisitiza kuwa mustakabali wa Afrika uko mikononi mwa Waafrika wenyewe, kupitia uongozi bora, ushirikiano, na matumizi sahihi ya rasilimali zake.”

Pia umuhimu wa kuwekeza katika uchakataji wa madini ndani ya nchi, ili kuongeza thamani, kuunda ajira, na kukuza uchumi wa viwanda huku akieleza tafiti zinaonyesha uwekezaji katika sekta hiyo unaweza kuongeza hadi dola bilioni 24 katika pato la taifa kwa mwaka na kuunda zaidi ya ajira milioni 2.3.

“Afrika inaongozwa na sera kama Africa Mining Vision na African Green Minerals Strategy, ambazo zinalenga kuimarisha viwanda, kuongeza thamani ya madini, na kuhakikisha maendeleo jumuishi. Pia, juhudi za kuanzisha minyororo ya thamani ya kikanda, kama ule wa betri na magari ya umeme unaoanzia Kongo na Zambia, zinaonyesha dhamira ya bara kujenga uchumi shindani.”

Amesema kupitia  mikakati ya pamoja na mifumo kama Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA), bara linaweza kubadilisha utajiri wake wa madini kuwa chanzo cha ustawi endelevu huku akisema Afrika inakadiriwa kumiliki karibu asilimia 30 ya hifadhi ya madini muhimu duniani.

Baadhi ya madini hayo cobalt, lithium, graphite na madini adimu (rare earth elements). Kwa mfano, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo huzalisha zaidi ya asilimia 70 ya cobalt duniani, huku nchi kama Zimbabwe, Mali, Tanzania na Msumbiji zikiwa na akiba kubwa ya lithium na graphite.

“Mahitaji ya madini haya yanatarajiwa kuongezeka kwa kasi ifikapo mwaka 2050, hasa kutokana na mabadiliko ya dunia kuelekea nishati safi. Hii inaipa Afrika fursa ya kipekee ya kukuza uchumi wake kupitia viwanda na kuongeza thamani ya rasilimali zake.”

Kuhusu changamoto ya uongezaji thamani amesema licha ya utajiri huo, sehemu kubwa ya madini ya Afrika husafirishwa nje yakiwa ghafi, hali inayopunguza manufaa ya kiuchumi kwa nchi husika. Inakadiriwa kuwa ni takribani asilimia 2 tu ya biashara ya madini hufanyika ndani ya bara la Afrika.

Wakati huo huo Waziri Mkuu wa zamani wa Ethiopia, Hailemariam Dessalegn, ameonya kuwa Afrika iko katika hatari ya kubaki maskini ikiwa itaendelea kuuza nje madini ghafi badala ya kuendeleza viwanda vya kuyachakata ndani ya nchi.

Amesisitiza bara hilo linaweza kukosa kunufaika na uchumi unaokua kwa kasi wa nishati safi licha ya utajiri wake mkubwa wa madini.Afrika ina akiba kubwa ya rasilimali muhimu kama vile cobalt, lithium, shaba na manganizi—madini muhimu kwa magari ya umeme, betri na mifumo ya nishati jadidifu.

Hata hivyo, madini mengi husafirishwa nje yakiwa ghafi, jambo linalopunguza ajira, ujuzi na ukuaji wa viwanda. Dessalegn alionya kuwa mpito wa nishati duniani unaweza kurudia mifumo ya kihistoria ambapo Afrika husambaza malighafi huku utajiri ukizalishwa kwingineko.







Na Mwandishi Wetu.

Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) imepokea ujumbe wa ngazi ya juu kutoka Serikali ya Shirikisho la Somalia kwa ajili ya mafunzo ya kujenga uwezo katika utumishi wa umma, hatua inayoonesha kuimarika kwa ushirikiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.

Mafunzo hayo yanafanyika katika Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) jijini Dar es Salaam, yakihusisha watumishi kutoka Idara ya Masuala ya Baraza la Mawaziri chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu wa Somalia. Lengo kuu ni kuimarisha mifumo ya uratibu wa serikali, usimamizi wa kumbukumbu, ulinganifu wa sera na ufuatiliaji wa maamuzi.

Hafla ya ufunguzi ilihudhuriwa na viongozi waandamizi wa serikali, akiwemo Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Xavier Daudi Mrope, aliyemwakilisha Serikali ya Tanzania.

Katika hotuba ya ufunguzi, Mkuu wa Chuo na Afisa Mtendaji Mkuu wa TPSC, Dr. Ernest Mabonesho alieleza kuwa mpango huo ni hatua muhimu katika kuimarisha taasisi za umma na kuongeza ufanisi wa utendaji wa serikali. Chuo hicho, kilichoanzishwa rasmi mwaka 2000 baada ya kuunganishwa kwa taasisi za mafunzo ya utumishi wa umma, kimeendelea kuwa kitovu cha ubora katika mafunzo, utafiti na ushauri wa kiutawala.

Imeelezwa kuwa mpango huo umeandaliwa kwa ombi la Serikali ya Somalia, kufuatia majadiliano kati ya TPSC na Ofisi ya Waziri Mkuu wa nchi hiyo. Mafunzo yanajumuisha nadharia, vitendo na uzoefu wa taasisi mbalimbali, yakilenga kuwapatia washiriki mbinu zitakazoweza kutumika katika kuboresha mifumo ya utawala nchini Somalia.

Mpango huo pia umeelezwa kuwa ni matokeo ya kuimarika kwa uhusiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Somalia, hasa baada ya ziara ya ngazi ya juu ya Serikali ya Tanzania nchini Somalia mwezi Desemba 2025, iliyoweka msingi wa ushirikiano katika maendeleo ya sekta ya umma.

Washiriki na viongozi wamebainisha kuwa mbali na kujenga ujuzi, mafunzo hayo yanatarajiwa kuimarisha mitandao ya kitaaluma na ushirikiano wa muda mrefu kati ya nchi hizo mbili.

Hatua hii inaonesha nafasi ya Tanzania katika kusaidia maendeleo ya taasisi za umma katika ukanda huu, huku nchi mbalimbali zikiongeza juhudi za kushirikiana kuboresha utawala na utoaji wa huduma kwa wananchi.

Mkuu wa Chuo na Afisa Mtendaji Mkuu wa TPSC, Dr. Ernest Mabonesho  akizungumza wakati wa   mafunzo ya kujenga uwezo watumishi wa Serikali ya Somalia  leo jijini Dar es Saam.
Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Xavier Daudi Mrope akiwa kwenye za pamoja
Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Xavier Daudi Mrope akizungmza wakati wa kufungua  mafunzo ya kujenga uwezo  kwa watumishi wa Serikali ya Somalia Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), jijini Dar es Salaam
Sehemu ya washiriki wa Mafunzo hayo.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amesisitiza umuhimu wa mshikamano wa Kitaifa ikiwa ni namna muhimu ya kuwaenzi waasisi wa Muungano, Hayati Baba wa Taifa Mwl. Julius Kambarage Nyerere na Hayati Abeid Amani Karume.

Makamu wa Rais ametoa msisitizo huo, wakati wa Tamasha la Usiku wa Mtanzania ikiwa ni shamrashamra za maadhimisho ya Miaka 62 ya Muungano, lililofanyika katika Ukumbi wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam.

Amesema ni msisitizo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa vijana na watanzania kwa ujumla kuhusu kuwa na mshikamano kulinda umoja na amani.

Makamu wa Rais amewasihi watanzania kutafakari na kujielekeza katika kujenga mshikamano ni kuhakikisha Muungano unalindwa.

Amesisitiza umuhimu wa kuvumiliana katika utoaji wa mawazo,kushauriana kujenga utaratibu wa kukubaliana hata katika masuala yanayotoafutiana mawazo.

Awali akitoa neno la utangulizi, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni amesema Tamasha hilo hilo linalenga amani, umoja na mshikamano miongoni mwa wananchi wa pande zote mbili za Muungano.

Amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi kwa kufanikisha kutatuliwa hoja 22 kati ya 25 za Muungano. Pia amempongeza Makamu wa Rais, kwa kuongoza Kikao cha Kamati ya Pamoja na kufanikisha kutatuliwa kwa hoja ya uingizaji sukari katika soko la Tanzania Bara hivyo kuufanya Muungano kuwa imara zaidi.

 Aidha, amesema shughuli mbalimbali zimefanyika katika Maadhimisho ya Miaka 62 ya Muungano, zikiwemo uzinduzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo, makongamano na mjidala kuhusu Muungano ikilenga kutoa elimu kwa wananchi.

 Aidha Serikali zote mbili kupitia Vyama vya Michezo zimeshirikiana katika kuandaa mashindano ya mpira wa miguu ya Kombe la Muungano yanayoendelea Zanzibar. Ameongeza kwamba, elimu ya Muungano itatolewa pia katika Msafara wa Muungano (Muungano Caravan) ambao utazinduliwa Mei 03, 2026 jijini Dar es Salaam na kuhusisha wilaya zote.










● Yawa kinara FDI , Miradi ya kimkakati yafungua ajira na mapato

Dodoma

Sekta ya Madini nchini imeendelea kudhihirisha ubora wake katika kuchangia uchumi wa Taifa baada ya kuongoza kwa kuvutia mtaji wa uwekezaji kutoka nje ya nchi (FDI), ambayo inachangia takribani robo tatu ya mtaji wote uliowekezwa katika sekta muhimu nchini.

Kwa mujibu wa Ripoti ya Uwekezaji Tanzania ya Mwaka 2025, thamani ya mtaji wa uwekezaji katika Sekta ya Madini imeongezeka hadi kufikia dola za Marekani bilioni 9.79 kwa mwaka 2024, kutoka dola bilioni 9.15 za mwaka 2023 na dola bilioni 8.64 za mwaka 2022.

Akiwasilisha Bungeni Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Madini kwa Mwaka wa Fedha 2026/27 Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde amesema kuwa, mazingira wezeshi yaliyowekwa na Serikali kwa wawekezaji yameendelea kuvutia wawekezaji wapya na kuwahamasisha waliopo kupanua miradi yao pamoja na kuwekeza zaidi kupitia faida wanazozipata

Waziri Mavunde amesema kuwa, katika kipindi cha mwezi Julai 2025 hadi Machi 2026 , bei ya dhahabu katika Soko la Dunia imepanda kwa kasi na kufikia wastani wa dola za Marekani 4,190.47 kwa wakia, ikilinganishwa na dola 2, 655.80 katika kipindi kama hicho mwaka uliotangulia.

Akielezea mwenendo wa biashara ya Madini ya Almasi Duniani imeendelea kushuka na kufikia wastani wa dola za Marekani 159.84 kwa karati, kutoka dola 168.95 kwa karati katika kipindi kama hicho mwaka 2024/25 , sawa na upungufu wa asilimia 5.39.

Aidha, Waziri Mavunde amebainisha kuwa, kushuka huko kunachangiwa na kuongezeka kwa uzalishaji wa almasi za viwandani( Synthetic diamonds) ambazo zimepunguza uhitaji wa almasi asilia katika masoko makubwa duniani ikiwemo China na Marekani.



















Top News