Na CHRISTOPHER LISSA

MKUU wa Wilaya ya Kisarawe, Petro Magoti, ametangaza operesheni kali dhidi ya wanaojihusisha na uvujaji wa mapato wilayani humo na kumwagiza Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya hiyo, Aidan Kitare, kuivunja kamati ya madiwani inayo husika na ukusanyaji wa mapato.

Aidha ametoa onya kali kwa baadhi ya madiwani watakao jaribu kulalamika baada ya kuondolewa au jamaa zao kuondolewa katika kamati hiyo kutokana na kubainika kushiriki katika kuhujumu mapato.

Magoti, aliyasema hayo alipohutubia kikao cha Baraza la Madiwani la Wilaya ya Kisarawe, mkoani Pwani, jana.

Alieleza kusikitishwa na uvujaji mkubwa wa mapato katika wilaya hiyo hali inayo kwamisha maendeleo.

"Watu wana kula kwelikweli. Wanakula vibaya mno halafu wanalalamika. Nataka niwaambie tumefahamiana kwa sababu ya kazi, tofauti na kazi sina udugu nanyie. Tufanye kazi , tumsaidie Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, kutekeleza majukumu,"alisema Magoti.

Alisema, dhamira ni kujenga Kisarawe inayo heshimu mali na mapato ya serikali ambapo kama mianya ya uvujaji wa mapato itadhibitiwa wilaya hiyo inaweza kukusanya sh.bilioni 7 tofauti na sh. bilioni 4 inazo kusanya sasa.

"Unakwenda sehemu unakuta waliumu wana kaa chini. Hawana ofisi. Hii ni aibu. Mapato yanaliwa na watu wachache,"alibainisha Magoti.

Alisema ana faili maalumu la wahusika wanao jihusisha kuhujumu mapato pamoja na maeneo yote yanayo tumika.

"Ninafaili hili hapa. Wahusika wote wanaohujumu mapato. Diwani ukiwa na malalamiko yoyote fika ofisini kwa Mwenyekiti wa Halmashauri au kwa mkurugenzi akulete kwa mkuu wa wilaya na ukibainika unahusika au ndugu yako unaye mtetea anahusika tukakupa ushahidi tutakuchukulia hatua,"alisema.

Alisema anataarifa za kila mtu aliyeondolewa katika Kamati ya Mapato ya halmashauri hiyo kupitia faili maalumu la wahujumu wa mapato.

"Diwani yoyote anaye jua kwamba ndugu yake alikula mapato taarifa zake ninazo humu katika falili.Diwani yoyote atakaye piga kelele nitamkamata,"alionya Magoti.

Alieleza, diwani kuwa na ndugu anaye kusanya mapato siyo dhabi bali dhambi ni kumtumia ndugu yake huyo kujipatia mapato na kuibia halmashauri.




"Kwa Mamlaka niliyo nayo ninakuelekeza mkurugenzi kuvunja kamati ya mapato hadi kufikia leo (jana) saa kumi alasili,"alisema.

pia alimtaka mkurugenzi huyo kukaa na Kamati ya Usalama ya wilaya hiyo kuunda kamati mpya kabla ya saa 12 jioni jana.

"Kamanti mpya ikiundwa, kesho (leo) wapewe semina, waingie kazini kutekeleza majukumu ya kukusanya mapato,"alieleza Magoti.

Aliongeza; "Na hiki mkurugenzi ndiyo kipimo chako cha kwanza cha kujua unatosha ama utoshoshi. Mimi ndiyo nina vyombo. Hakuna mtu yoyote mwenye vyombo katika wilaya hii. Mkurugenzi usiogope. Mimi ndiyo naweza kusema uwepo au usiwepo kwa hiyo fanya kazi,"

Aidha alielekeza polisi wilayani humo kumsakama mmiliki mmoja wa jengo la ghorofa jirani na ofisi za halmashauri hiyo ambalo alisema lina husika katika vitendo vya kuhujumu mapato.

"Kuna kijengo cha ghorofa jirani na hapa halmashauri. Mwiteni mmiliki anieleze shughuli zinazofanyika pale hadi saa saba usiku na kuanza kesho usiku (leo) wote watao kuwa pale wakamatwe,"alisema.

Alisema mmiliki wa jengo hilo ambaye ni mwanamke afikishwe mbele yake kabla ya saa 9:00 alasili jana kujieleza.

Katika hatua nyingine, Magoti alitangaza kufanya operesheni ya kuvunja nyumba zilizojengwa kinyume cha sheria katika eneo la serikali la Homboza na kwamba katika operesheni hiyo aliyo ibatiza jina la Kanyamazongo atawatia mbaloni mabalozi saba wanaopinga jitihada za serikali.

"Hatuhitaji watu wanao hujumu serikali.Pale halmashauri itaingiza shilingi bilioni 5.8. Kuna shule imejengwa pale halmashauri ili nunua eneo lake yenyewe.Ni vitu vya ajabu sana,"alisema.

Aidha Magoti alitaja vizuizi vinavyoongoza kwa kuiba mapato wilayani humo na kuyatorosha kuwa ni Homboza, Kwa Pinda, Kiluvya Kisokwa, Ikuruwi, Kauzeni, Msanga na Masaki.

" Kuna watu wanachukua fedha taslimu pale.Tunaorodha yao humu katika faili. Tutakamata baiskeli, pikipi, magari na kila muhusika,"alisema Magoti.

Kuhusu watu wanaouza kiholela maeneo hususan katika eneo la Cha Kenge, Magoti alisema Operesheni Kanyazongo itamkumba kila muhusika.

"Madiwani niwaombe nyie ndiyo viongozi wa kamati za maendeleo za kata kwa hiyo kama eneo lako linauza viwanja kinyume cha utaratibu tutakuhoji,"alisema.



















Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Mhe. Godfrey Eliakimu Mnzava, akiwa ameambatana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya, viongozi wa siasa, pamoja na timu ya wataalamu wa Halmashauri ya Wilaya ya Moshi, amefanya ziara ya kikazi kutembelea na kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo iliyopendekezwa kupitiwa na Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2026.

Katika ziara hiyo, Mhe. Mnzava alikagua mradi wa Kituo cha Mafuta cha Mavoa kilichopo Kitongoji cha Njiapanda Magharibi, Kata ya Njiapanda, pamoja na mradi wa Zahanati ya Ghona uliopo Kijiji cha Ghona katika Kata ya Kahe Mashariki. 

Aidha, Mkuu wa Wilaya na timu yake walifika katika Shule ya Sekondari Mwika ambapo ndipo litakapokuwa eneo la mapokezi ya Mbio za Mwenge wa Uhuru 2026, eneo ambalo pia Mwenge utajionea programu maalum ya matumizi ya Nishati Safi.

Miradi mingine iliyofanyiwa ukaguzi ni pamoja na ujenzi wa barabara katika Kata ya Kilema Kusini, mradi wa maji wa Kijiji cha Mabungo uliopo Kata ya Kirua Vunjo Kusini, pamoja na mradi wa vijana na uzalishaji wa madini ya ujenzi. 

Vilevile, ziara hiyo ilihusisha ukaguzi wa ujenzi wa Ofisi ya Kata ya Kimochi na ujenzi wa Shule ya Amali ya Sekondari Chemchem iliyoko Manushi katika Kata ya Kibosho Magharibi.

Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa mwaka 2026 zinatarajiwa kuingia mkoani Kilimanjaro tarehe 28 Juni 2026 na kukimbizwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Moshi ifikapo tarehe 01 Julai 2026. 

Mwenge huo utaongozwa na kaulimbiu isemayo: “Tanzania ni Yetu Sote, Tushikamane kwa Pamoja Kuleta Maendeleo.









Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Kahama, Stephen Magalla, akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo kwa watoa huduma za afya yaliyoandaliwa kwa lengo la kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia (GBV) na ukatili dhidi ya watoto (VAC) katika Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.


Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Kahama, Stephen Magalla, akifungua mafunzo ya kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia (GBV) na ukatili dhidi ya watoto (VAC) kwa watoa huduma za afya katika Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, Shinyanga.

**Shirika la Tanzania Health Promotion Support (THPS), kwa kushirikiana na Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali (GCLA) na kwa ufadhili wa Sanlam Allianz, limeanza rasmi kuendesha mafunzo ya kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia (GBV) na ukatili dhidi ya watoto (VAC) katika Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.

Mafunzo haya yanatekelezwa kupitia Mradi wa Paza Sauti+ unaolenga kuiwezesha jamii kuzungumza wazi dhidi ya ukatili huku ukijenga uwezo wa watoa huduma za afya katika ukusanyaji na matumizi sahihi ya ushahidi wa kiforensiki.

Mradi wa Paza Sauti+ unalenga kuimarisha uwezo wa kiforensiki kwa uchunguzi unaotegemea ushahidi, kuhamasisha kutoa taarifa za matukio kwa wakati na kwa usalama, kuongeza uelewa wa umuhimu wa ushahidi wa vinasaba (DNA) katika upatikanaji wa haki na kuimarisha uratibu kati ya sekta za afya, polisi na ustawi wa jamii.

Mafunzo kwa watoa huduma wa afya yanafanyika kuanzia tarehe 5 hadi 7 Mei 2026, yakifuatiwa na mafunzo maalum kwa Wahudumu wa Afya ya Jamii (CHWs) tarehe 8 Mei 2026.

Lengo ni kuimarisha mifumo ya utambuzi wa mapema, uripoti wa matukio, ukusanyaji wa ushahidi na utoaji wa huduma bora kwa manusura.

Kupitia mafunzo haya, washiriki wanapatiwa ujuzi wa kutambua matukio ya ukatili mapema, Kuripoti kwa wakati na kwa usahihi, kukusanya na kuhifadhi ushahidi wa kiforensiki ipasavyo na kutoa huduma zinazomlenga manusura

Akizindua rasmi mafunzo hayo, Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Kahama, Stephen Magalla, amepongeza ushirikiano kati ya THPS, GCLA na Sanlam Allianz.

“Ushirikiano huu unaakisi mwitikio shirikishi unaohitajika katika kukabiliana na ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto. Kuimarisha mifumo ya kiforensiki na uwezo wa watoa huduma kutaboresha kwa kiasi kikubwa msaada kwa manusura na kuhakikisha wanapata haki kwa wakati,” amesema Magalla.

Kwa upande wake, Ndugu Julius Magabe, Mtendaji Mkuu wa Sanlam Allianz Life Insurance Tanzania, alisisitiza dhamira ya kampuni hiyo katika kuunga mkono mradi wa Paza Sauti+.

“Tunajivunia kuwa sehemu ya mradi huu muhimu. Tumeamua kuunga mkono Mradi wa Paza Sauti+ kama mchango wetu katika kupunguza na kupambana na ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto. Kama taasisi inayolinda maisha kupitia huduma za bima, tunatambua umuhimu wa kuunga mkono juhudi zinazolinda ustawi na heshima ya jamii.”

Washiriki wa mafunzo ni pamoja na watoa huduma za afya, maafisa wa dawati la jinsia kutoka Jeshi la Polisi, maafisa ustawi wa jamii na wadau wa kijamii.

Mafunzo haya yanawawezesha kuimarisha mchango wao katika mnyororo mzima wa kushughulikia masuala ya ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto, kuanzia utambuzi wa mapema hadi usimamizi wa kesi.

Uzinduzi huo umehudhuriwa na viongozi wa serikali wa ngazi ya mkoa, ukiashiria dhamira thabiti ya kisiasa na taasisi katika kukabiliana na vitendo vya ukatili na kuboresha upatikanaji wa haki kwa manusura.

Aidha, katika hafla hiyo walikuwepo pia Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (OC-CID) Kahama, SP Maro Kenyunko, pamoja na Afisa Ustawi wa Jamii wa Halmashauri ya Mji wa Kahama, Abrahamani Kibakaya, ambao wameipongeza THPS, GCLA na Sanlam Allianz kwa hatua za wakati muafaka katika kuziba mapengo yaliyopo kwenye kushughulikia masuala ya ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto kupitia Mradi wa Paza Sauti+.

Wadau wamebainisha changamoto zinazoendelea katika ukusanyaji na matumizi ya ushahidi wa kiforensiki, hali inayochangia kuchelewesha au kudhoofisha mashauri ya ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto.

Mradi huu unalenga kuziba mapengo hayo kwa kujenga uwezo wa kitaalamu na kuongeza uelewa wa jamii juu ya umuhimu wa kuripoti mapema.

Mradi wa Paza Sauti+ unatekelezwa katika Hospitali ya Wilaya ya Kahama na Kituo cha Afya Nyasubi, ukihusisha kata za Nyasubi na Malunga, ukiendana na Mpango wa Kitaifa wa Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto (NPA-VAWC II).

Kwa kuimarisha mifumo na ushiriki wa jamii, Mradi wa Paza Sauti+ unalenga kuhakikisha manusura wanasikilizwa, wanapatiwa huduma bora kwa wakati, na wanapata haki stahiki.

THPS pia inaipongeza Sanlam Allianz kwa mchango wake katika kupambana na ukatili kupitia programu za uwajibikaji kwa jamii.


Kuhusu THPS


Tanzania Health Promotion Support (THPS) ni shirika lisilo la kiserikali lililosajiliwa nchini, linalojikita katika kuboresha upatikanaji wa huduma bora za afya na ustawi wa jamii kwa Watanzania wote. Tangu mwaka 2011, THPS imekuwa ikishirikiana na Serikali ya Tanzania kuimarisha mifumo ya afya na jamii kupitia mbinu mbalimbali zinazotegemea Ushahidi wa kisayansi.


Kuhusu Paza Sauti+


Mradi wa Paza Sauti+ ni mpango unaoshirikisha Serikali na sekta binafsi unaolenga kuimarisha sauti za jamii, kujenga uwezo wa taasisi, na kuboresha upatikanaji wa haki kwa manusura wa ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto nchini Tanzania.

Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Kahama, Stephen Magalla, akifungua mafunzo ya kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia (GBV) na ukatili dhidi ya watoto (VAC) kwa watoa huduma za afya katika Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, Shinyanga.

Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Kahama, Stephen Magalla, akifungua mafunzo ya kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia (GBV) na ukatili dhidi ya watoto (VAC) kwa watoa huduma za afya katika Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, Shinyanga.

Mganga Mkuu Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, Dkt. Baraka Msumi akizungumza kwenye mafunzo ya kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia (GBV) na ukatili dhidi ya watoto (VAC) kwa watoa huduma za afya katika Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, Shinyanga.

Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (OC-CID) Kahama, SP Maro Kenyunko akizungumza kwenye mafunzo ya kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia (GBV) na ukatili dhidi ya watoto (VAC) kwa watoa huduma za afya katika Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, Shinyanga.

Afisa Sheria kutoka Ofisi ya Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Mohamed Mdemu akizungumza kwenye mafunzo ya kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia (GBV) na ukatili dhidi ya watoto (VAC) kwa watoa huduma za afya katika Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, Shinyanga.

Mratibu wa Mradi wa Paza Sauti + kutoka Shirika la Tanzania Health Promotion Support (THPS), Agnes Kirato akielezea mradi wa Paza Sauti +

Mratibu wa Mradi wa Paza Sauti + kutoka Shirika la Tanzania Health Promotion Support (THPS), Agnes Kirato akielezea mradi wa Paza Sauti +

Mratibu wa Mradi wa Paza Sauti + kutoka Shirika la Tanzania Health Promotion Support (THPS), Agnes Kirato akielezea mradi wa Paza Sauti +











Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma 

Rais wa Kenya, William Ruto, amesema kuwa uhusiano kati ya Tanzania na Kenya si wa kawaida bali ni wa kipekee na wa kihistoria, uliosimikwa katika misingi ya ujirani wa moja kwa moja, udugu wa kitamaduni na lugha inayowaunganisha wananchi wa mataifa hayo mawili ya Afrika Mashariki.

Akihutubia Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jijini Dodoma leo, Rais Ruto alieleza kuwa mahusiano kati ya nchi hizo mbili hayawezi kupimwa kwa jicho la kisiasa pekee, bali yanapaswa kueleweka kama uhusiano wa asili uliowekwa na historia na maisha ya kila siku ya wananchi wanaoishi mpakani.

Alisisitiza kuwa Tanzania na Kenya ni majirani wa kudumu waliounganishwa na jiografia na pia uhusiano wa kijamii unaovuka mipaka ya kisiasa, jambo ambalo linapaswa kulindwa na kuendelezwa kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Ruto alitumia methali maarufu isemayo, “unaweza kuchagua rafiki, lakini jirani unapatiwa na Mungu,” akibainisha kuwa ujirani huo ni zawadi inayopaswa kuendelezwa kwa amani, heshima na ushirikiano wa karibu kati ya mataifa hayo mawili.

Aidha, Rais huyo wa Kenya alieleza kuwa Tanzania na Kenya tayari zinashirikiana kwa kiwango kikubwa katika nyanja mbalimbali za kijamii, kiutamaduni na kiuchumi. Alitaja matumizi ya pamoja ya lugha ya Kiswahili kama mojawapo ya nguzo muhimu inayowaunganisha wananchi wa pande zote mbili.

Pia alizungumzia uwepo wa jamii zinazovuka mipaka ya nchi, kama Wamaasai na Wakuria, ambazo zimeendelea kuimarisha uhusiano wa kifamilia na kitamaduni kati ya Kenya na Tanzania, hivyo kufanya mipaka ya kisiasa isiwe kikwazo cha udugu wao wa muda mrefu.

Ruto aliongeza kuwa mshikamano huo wa asili unapaswa kuwa msingi wa kuimarisha zaidi ushirikiano katika sekta za uchumi, biashara, uwekezaji, elimu na miundombinu ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Kwa mujibu wake, endapo nchi hizo mbili zitaendeleza mshikamano huo kwa vitendo, wananchi wa Tanzania na Kenya watanufaika moja kwa moja kupitia ongezeko la fursa za ajira, biashara na maendeleo ya kijamii, hatua ambayo itaimarisha zaidi ustawi wa ukanda mzima wa Afrika Mashariki.

Rais Ruto alihitimisha kwa kusisitiza kuwa mustakabali wa mataifa ya Afrika Mashariki upo katika mshikamano, kuondoa vikwazo visivyo vya lazima na kuimarisha ushirikiano unaoweka wananchi mbele kama walengwa wakuu wa maendeleo ya kikanda.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiagana na Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Dkt. William Samoei Ruto mara baada ya kuhitimisha Ziara yake ya Kitaifa, katika viwanja vya Gwaride Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 05 Mei, 2026.


Maadhimisho ya siku ya Urithi wa Dunia Afrika yaliyofanyika katika Makumbusho ya Urithi Jiopaki mjini Karatu tarehe 5 Mei, 2026 yameyakutanisha makabila makuu manne yanayounda Jiopaki ya Ngorongoro Lengai ambayo ni wamasai, wahadzabe, wairaqw na wadatoga na hivyo kuunganisha kutaniko kubwa la urithi wa dunia katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Mkuu wa wilaya ya Karatu Mhe. Dkt Lameck Karanga amesema uwepo wa makabila hayo, historia yao pamoja na kuenzi tamaduni zao ni utajiri mkubwa kwa Tanzania na kutoa wito kwa wadau na jamii kwa ujumla kuendelea kulinda maeneo ya urithi wa dunia na kuibua maeneo mapya yatakayoingizwa katika orodha ya Urithi wa Dunia ili kuongeza thamani ya ubora wa kipekee ulimwenguni (Outstanding Universal Value) na kuvutia wageni wengi zaidi.

Naibu Kamishna wa Uhifadhi, Utalii na Maendeleo ya Jamii Ngorongoro Joas Makwati ameeleza kuwa mamlaka itaendelea kuongeza juhudi za kulihifadhi eneo la Ngorongoro ambalo ni urithi wa dunia na kultangazia zaidi kama eneo pekee lenye Ushahidi wa kisayansi kuhusu historia ya binadamu unaoeleza kuwa binadamu kwa kuthibitishwa na ugunduzi wa masalia ya binadamu wa kale na zana za mawe zilizopatikana katika bonde la Olduvai.

Kwa upande wake Naibu Katibu wa Tume ya Taifa ya UNESCO Tanzania Dkt. Khamis Said ameeleza kuwa tangu Tanzania ijiunge na UNESCO imepata mafanikio mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuridhia mikataba kumi (10) ya UNESCO,Kuwepo kwa Hifadhi Hai za Mwanadamu na Mazingira sita (6) na Kuwepo kwa maeneo saba (7) ya urithi wa Dunia.

Kauli mbiu ya siku ya urithi wa dunia kwa mwaka huu ni “Kusherekea siku ya Urithi wa Dunia na kukuza Viongozi wa baadaye”. (Celebrating Africa’s Heritage, Mentoring the Leaders of Tomorrow).












Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Mshambuliaji wa zamani wa Timu ya Taifa ya Ivory Coast na Timu ya Chelsea ya Uingereza Didier Drogba mara baada ya kuwasili Ikulu Chamwino mkoani Dodoma, tarehe 05 Mei, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Mshambuliaji wa zamani wa Timu ya Taifa ya Ivory Coast na Timu ya Chelsea ya Uingereza Didier Drogba mara baada ya kuwasili Ikulu Chamwino mkoani Dodoma, tarehe 05 Mei, 2026. Katika mazungumzo yao Mhe. Rais Dkt. Samia amemuomba Nyota huyo Ivory Coast kuwa Balozi wa Tanzania kuelekea Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) mwaka 2027.

Aidha, Rais Dkt. Samia ameitaka Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kushirikiana na mchezaji huyo kubadilishana uzoefu wa kuendesha Vituo vya michezo nchini (Sports Academy). Mchezaji huyo amemshukuru Rais Dkt. Samia na kuonesha utayari wa kushirikiana na Serikali. Pamoja na mafanikio kadhaa aliyoyapata katika Mpira wa miguu, Mwaka 2005, alifanya ushawishi uliosaidia kusitishwa kwa vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini kwao vilivyodumu kwa miaka kadhaa.


 

 Na Karama Kenyunko Michuzi Tv

OFISA Uchunguzi wa Halotel Fabian Kulwa (40) na wenzane watano wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na mashtaka 28 ikiwemo kutumia namba za NIDA za wateja kusajilia laini za watu wengine na kutakatisha fedha Sh milioni 355. Mbali na Kulwa anayeishi Mbezi Makabe washtakiwa wengine ni Gilbert Nyamitah (33) Mkazi wa Madale, Mnyamisi Selumamala (34), Mkazi wa Musoma Mara, Salum Kapene (31) Ofisa Masoko wa Halotel Mkazi wa Mwanza, Onesmo Aron (34) mfanyakazi huduma huru Mkazi wa Runzewe Geita na Joram Fanuel (23) Mkazi wa Tarime Mara. Watuhumiwa hao wakiongozwa na mshtakiwa wa kwanza Nyamitah ambae ni mlemavu wa miguu anayetumia kiti cha magurudumu wamesomewa mashtaka yao mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu Beda Nyaki. Akisoma hati ya mashtaka Wakili wa Serikali Michael Shindai amedai kuwa washtakiwa wanadaiwa kutenda makosa hayo kati ya Mei, Julai, 2025 na Aprili 2026 ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Amedaiwa washtakiwa wanatuhumiwa kwa kosa la kuongoza genge la uhalifu, kutumia laini iliyosajiliwa kwa jina la mtu mwingine, kutumia vibaya taarifa za mteja na kutakatisha fedha. Imedaiawa katika shtaka la kwanza la kuongoza genge la uhalifu, washtakiwa wote, kati ya Mei Mosi, 2025 katika mahali pasipojulikana ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa makusudi waliongoza genge la uhalifu kwa kutumia taarifa za wateja na laini za simu zilizokuwa na usajili wa watu wengine. Katika shtaka la pili hadi la 18 mshtakiwa Nyamitah anaiwa, Machi 31,2026 alitumia laini zilizosajiliwa kwa jina la mtu mwingine akiwa Madale ndani ya Wilaya Kinondoni mkoa wa Dar es Salaam bila ya kumjulisha mtoa huduma. Imedaiwa kuwa alitumia laini iliyosajiliwa kwa jina la Kwimba Maduhu, Bhoke Ryoba, Daniel Ng'era, Chacha Mbango, Zainabu Burunya, Manga Marwa, Bhoke Mwita, Verynice Nyaonge, Masele Kinga, Charles Genga na Latifa Athumani. Wakili Shindai aliendelea kudai kuwa katika shtaka la 19 hadi 27 mshtakiwa Majige, akiwa mfanyakazi huru wa Kampuni ya Honora Tanzania PLC alitumia namba ya NIDA ya Tagambi Bungulwa kusajili namba 0714-643547 kosa analodaiwa kulitenda Mei Mosi, 2025 huko Wilaya Busega mkoani Simiyu Pia, anatuhumiwa kutumia namba za watu wengine za NIDA za Joseph Mwita, Bhoke Mwita, Manga Marwa, Kwimba Maduhu, Bhoke Roba, Daniel Ng'era, Chacha Mbango na Zainabu Burunya. Katikati shtaka la utakatishaji fedha, Nyamitah na Kulwa wanadaiwa wakiwa mahali pasipojulikan ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa pamoja walifanikiwa kupata Sh milioni 355 huku wakijua fedha hizo ni mazalia ya kosa la uhalifu wa kutumia laini za simu zilizosajiliwa kwa majina ya watu wengine. Hata hivyo, washtakiwa hawakutakiwa kujibu chochote kwa sababu Mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo, ambapo upande wa Jamhuri ulidai kuwa upelelezi bado haujamilika. "Mshtakiwa wa kwanza (Nyamitah) na wa pili (Kulwa) nyie hamna dhamana kwa sababu mna shtaka la utakatishaji fedha, mliyobaki kila mmoja anatakiwa awe na wadhami wawili kila mmoja atasaini bondi ya Sh milioni tano,"amesema Hakimu Nyaki Kesi hiyo imeahirishwa hadi Mei 18, mwaka huu kwa ajili ya kutajwa.




 

*Watoto wanaolazwa wapungua kutoka 32 hadi 7 kwa robo mwaka

Na Augusta Njoji

IDADI ya watoto wanaokabiliwa na utapiamlo mkali katika Halmashauri ya Mji Handeni imepungua kwa kiasi kikubwa, kutoka watoto 32 waliokuwa wakilazwa hospitalini kwa robo mwaka 2024/25 hadi wastani wa watoto watano hadi saba kwa robo mwaka 2025/26.

Mafanikio hayo yanatajwa kuchangiwa na mikakati madhubuti ya utoaji elimu ya lishe kwa jamii inayotekelezwa na Hospitali ya Halmashauri hiyo, ikilenga kupunguza lishe duni hususan kwa watoto.

Akizungumza Mei 5, 2026 katika kikao cha tathmini ya shughuli za lishe kwa kipindi cha Januari hadi Machi 2025/26, Afisa Tarafa ya Chanika, Julieth Mushi, akimwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, amepongeza juhudi hizo na mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa mkataba wa lishe.

Amesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Idara ya Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe pamoja na Idara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi katika kuhamasisha jamii kuanzisha bustani za mboga majumbani na kufuga wanyama ili kukabiliana na tatizo la utapiamlo kwa watoto.

Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Halmashauri hiyo, Dkt.Hudi Shehdadi, amesema mikakati inayoendelea kutekelezwa ni pamoja na kushirikiana na Idara za Elimu ya Msingi na Sekondari pamoja na kamati za lishe za kata kuhamasisha upandaji wa miti ya matunda na uanzishaji wa bustani za mboga, huku kila shule ikitakiwa kutenga angalau hekari mbili kwa ajili ya kilimo cha mahindi.

Aidha, amebainisha kuwa juhudi zimeongezwa katika kuhamasisha wajawazito kuhudhuria huduma za afya mapema ili kupata elimu ya lishe pamoja na virutubisho vya madini chuma, hatua inayolenga kupunguza idadi ya watoto wanaozaliwa na uzito pungufu.

Awali, akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za lishe kwa kipindi cha Januari hadi Machi 2025/26, Kaimu Afisa Lishe wa Halmashauri hiyo, Getruda Kasabaja, amesema jumla ya wazazi na walezi 9,571 wamefikiwa na elimu ya lishe, huku watoto 17,390 wakifanyiwa tathmini ya hali ya lishe.

Ameeleza kuwa kati ya watoto hao, watoto 221 walikuwa na uzito pungufu sawa na asilimia 1.27, watoto 80 walikuwa na udumavu (asilimia 0.4), na watoto 96 walikuwa na ukondefu (asilimia 0.55). Aidha, watoto saba walipatiwa matibabu ya utapiamlo mkali katika kipindi hicho.


Top News