Na Mwandishi Wetu

Baraza la Ushindani Halali Zanzibar (ZFCT) limefanya ziara ya mafunzo katika Tume ya Ushindani ya Haki (FCC) kwa lengo la kujifunza na kubadilishana uzoefu katika masuala ya ushindani wa biashara, udhibiti wa bidhaa bandia pamoja na usimamizi wa mashauri yanayohusiana na ushindani.

Ziara hiyo iliyofanyika katika ofisi za FCC Juni 10, 2026 Jijini Dar es Salaam, imeelezwa kuwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi hizo mbili ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao na kuhakikisha mazingira ya biashara yanakuwa ya haki kwa wadau wote.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi. Khadija Ngasongwa alisema kuwa kubadilishana uzoefu na taasisi za ndani ya nchi ni muhimu katika kuimarisha mifumo ya usimamizi wa ushindani na kulinda maslahi ya watumiaji dhidi ya vitendo vinavyokiuka sheria za ushindani na biashara.

Alisema ujumbe wa ZFCT unapata fursa ya kujifunza namna FCC inavyotekeleza majukumu yake ya kudhibiti vitendo vya ushindani usio wa haki, kukabiliana na biashara ya bidhaa bandia pamoja na mifumo ya uchunguzi na uendeshaji wa mashauri mbalimbali yanayofikishwa mbele ya taasisi hiyo.

Kwa upande wake, ujumbe wa ZFCT ukiongozwa na Msajili wa Baraza, Bi. Fatma Yahya alieleza kuridhishwa na mafunzo na uzoefu uliopatikana katika ziara hiyo, ukibainisha kuwa utaisaidia taasisi hiyo kuimarisha utendaji wake katika kushughulikia rufaa na mashauri yanayohusiana na ushindani wa biashara Zanzibar.

ZFCT ni chombo kinachoshughulikia mashauri na rufaa zinazotokana na maamuzi ya mamlaka za ushindani, ambapo wadau wasiokubaliana na maamuzi yaliyotolewa huwasilisha kesi zao kwa ajili ya kusikilizwa na kutolewa uamuzi.

Ziara hiyo pia ilitoa nafasi kwa wataalamu kutoka pande zote mbili kujadiliana changamoto na fursa zilizopo katika usimamizi wa ushindani wa biashara, huku wakisisitiza umuhimu wa kuendelea kushirikiana katika kujenga uwezo wa kitaasisi na kuimarisha utekelezaji wa sheria zinazolinda ushindani wa haki katika soko.

DODOMA Jiji wametwaa ubingwa wa jumla wa mashindano ya UMISSETA ngazi ya mkoa 2026 baada ya kuonyesha kiwango cha juu cha ushindani na kujikusanyia alama 255 zilizowahakikishia nafasi ya kwanza.

‎Ushindi huo umechangiwa na mwendelezo mzuri wa matokeo katika michezo mbalimbali ambapo wamenyakua vikombe 10, ikiwemo mpira wa kikapu (wavulana na wasichana), mpira wa mikono (wavulana na wasichana), mpira wa wavu wavulana, soka wasichana na kizazi kipya, huku wakimaliza nafasi ya pili katika mpira wa wavu wasichana.

‎‎Akizungumzia ushindi huo, Afisa Elimu Sekondari wa Jiji la Dodoma, Mwl. Daniel Mapilya, alisema mafanikio hayo yameambatana na uwakilishi mkubwa katika timu ya mkoa, ambapo kati ya wanafunzi 120 waliochaguliwa, 45 wametoka Jiji la Dodoma, hatua inayoonesha ubora wa maandalizi kuelekea mashindano ya kitaifa yatakayofanyika Iringa.

“Mafanikio hayo ni makubwa kwa jiji letu, na tunawapongeza walimu wa michezo, wakuu wa shule, maafisa utamaduni na michezo pamoja na maafisa elimu sekondari kwa mchango wao mkubwa uliowezesha ushindi huu kupatikana” alisema Mwl. Mapilya.

‎Nae, Afisa Michezo wa Jiji la Dodoma, Peter Ititi alisema mafanikio hayo yamechangiwa na ushirikiano mzuri kutoka kwa Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma na Mbunge wa Jimbo la Mtumba ambao wamekuwa wakiwapa hamasa. Aliahidi kuwa wataendelea kufanya vizuri na kuongeza idadi ya makombe katika mashindano yajayo.

‎‎Kwa upande wake, Mchezaji wa Mpira wa Miguu wa Dodoma Jiji, Fortunata Mfaume aliyeteuliwa kuwakilisha timu katika mashindano ya kitaifa yatakayofanyika mkoani Iringa, alisema kuwa amejipanga kikamilifu kuhakikisha anatoa mchango wake kwa timu ya mkoa na kuiwezesha kufanya vizuri katika mashindano hayo.

‎Mafanikio ya Dodoma Jiji katika mashindano ya UMISETA ngazi ya mkoa 2026 yanadhihirisha maandalizi mazuri, mshikamano na ushindani wa hali ya juu. Timu hiyo sasa inaelekeza macho yake katika mashindano ya kitaifa, ikilenga kuendeleza rekodi yake ya ubabe kimichezo.







Wakulima nchini wametakiwa kutumia mbegu bora wanapopanda mazao yao ili kuongeza uzalishaji wa mazao yenye ubora wa juu yatakayowezesha kupata bei nzuri kwenye masoko ya ndani na nje ya nchi.

Wito huo umetolewa na Afisa Mtendaji Mkuu wa Soko la Bidhaa Tanzania (TMX), CPA. Godfrey Malekano, wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari kutoka mikoa ya Dar es Salaam, Dodoma, Iringa na Singida yaliyofanyika jijini Dodoma Juni 12, 2026.

CPA. Malekano alisema ubora wa mazao ndiyo msingi mkuu wa upatikanaji wa bei nzuri sokoni, akisisitiza kuwa matumizi ya mbegu bora ni hatua muhimu kwa mkulima kufikia mafanikio ya kiuchumi.

Alisema utaratibu wa wanunuzi kununua mazao moja kwa moja mashambani bila kuyapeleka kwenye mfumo rasmi wa soko umepitwa na wakati, kwani kwa sasa wakulima wana fursa ya kupata bei shindani kupitia mfumo wa TMX uliorasimishwa na Serikali.

“Unapouza mazao nje ya mfumo rasmi, si mkulima pekee anayepoteza fursa ya kupata thamani halisi ya mazao yake, bali hata Serikali inapoteza matokeo ya uwekezaji wake mkubwa katika utoaji wa pembejeo za ruzuku kwa wakulima."

Aliongeza kuwa TMX inaendelea na jitihada za kuhakikisha bidhaa zote za kilimo zinauzwa kupitia soko hilo kama ilivyo katika mataifa mengi yaliyoendelea, Kwa sasa, bidhaa 11 tayari zinauzwa kupitia mfumo huo ikiwemo madini ya Vito.

Aidha, alisema maendeleo ya teknolojia yameongeza uelewa wa wakulima kuhusu mwenendo wa bei za mazao katika soko la dunia kupitia matumizi ya simu janja, hali inayowasaidia kufanya maamuzi sahihi ya biashara.

“Leo hii mkulima anafuatilia bei za mazao akiwa kijijini kupitia simu yake, ndiyo maana wanunuzi wanaotaka kununua kwa bei ya chini hukataliwa kwa sababu wakulima wengi wanatambua thamani halisi ya mazao yao."

Kwa upande wake, Ofisa wa TMX, Justa Martine, alisema kuuza mazao kupitia Soko la Bidhaa Tanzania kuna manufaa makubwa kwa wanunuzi na wauzaji.

Alieleza kuwa mfumo huo hupunguza gharama za mnunuzi kufika eneo la mzigo, huongeza uwazi wa biashara kwa kuonyesha ubora wa bidhaa na mwenendo wa bei sokoni, na pia humpa muuzaji uhuru wa kukubali au kukataa kuuza endapo hajaridhishwa na bei inayotolewa.

TMX inaendelea kuhamasisha wakulima na wadau wa sekta ya kilimo kutumia mfumo wa soko la bidhaa ili kuongeza tija, uwazi na ushindani katika biashara ya mazao nchini.




Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa - TAKUKURU Mkoa wa Geita, imewafikisha mahakamani watumishi wa umma saba kwa tuhuma za ubadhirifu wa fedha za Serikali zaidi ya Sh milioni 78.

Akizungumza na wanahabari leo Juni 12, 2026, Mkuu wa TAKUKURU Geita amesema watumishi hao walikusanya mapato kupitia mfumo wa LGRCIS kwa kutumia mashine za POS lakini hawakuwasilisha fedha hizo katika akaunti ya Serikali.

"Uchunguzi umebaini watumishi hao walisababisha Serikali kupata hasara ya jumla ya Sh78,875,110/= kinyume na utaratibu," amesema.

Watumishi hao ni: Tatu Jeki Kijungu - Afisa Hesabu Wilaya ya Geita, Sylvanus Ngoya Michael - Mhasibu Wilaya, Ladislaus Katuma Kamhanda - Afisa Mtendaji Kata Nyamalimbe, Melina Damian Buguba - Afisa Uvuvi, Mtani Daniel Yangwe na Allen Michael Kimaro - Makusanya Mapato Manispaa, na Mashalla Charles Nkwande - Afisa Mtendaji Kata Kakubilo.

Baada ya kupata vibali kutoka Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, mashauri 7 yamefunguliwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita leo kwa nambari ECO.13145/2026 hadi ECO.13153/2026.



 

Wakulima wa zao la pamba kutoka vijiji vya Mbutu, Iyogelo, Ilambakuki, Imalanguzu na Mwamakoma vilivyopo katika Wilaya ya Igunga, Mkoa wa Tabora, wamehamasika kufungua akaunti za benki na kusajili laini za simu ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kupokea malipo ya mazao yao kwa njia ya kidijitali. Hatua hiyo inalenga kuongeza uwazi, usalama na uharaka wa malipo kwa wakulima.

Wakulima hao wamefungua akaunti kupitia Benki ya NMB pamoja na kusajili laini kupitia mtandao wa simu wa Mixx by Yas, hatua itakayowawezesha kupokea fedha zao kwa urahisi kupitia mifumo ya benki na huduma za kifedha za simu za mkononi.

Zoezi hilo limefanyika kwa kushirikiana na AMCOS za Ngw'ajojabi, Ngw'asabi na Mwamakoma AMCOS, likitekelezwa kufuatia waraka wa Mrajis wa Vyama vya Ushirika unaoelekeza malipo ya wakulima wa pamba kufanyika kupitia akaunti za benki na huduma za fedha kwa njia ya simu badala ya kutegemea fedha taslimu. Lengo ni kuhakikisha wakulima wanapata malipo yao kwa wakati, kwa uwazi na kwa usalama zaidi.

Mwitikio wa wakulima umeendelea kuongezeka siku hadi siku kufuatia juhudi za uhamasishaji zinazoendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali. Hadi kufikia Juni 10, 2026, jumla ya wakulima 506 wamejitokeza na kufungua akaunti pamoja na kujiunga na huduma za kifedha za simu, hatua inayoonesha uelewa na utayari mkubwa wa wakulima kupokea mabadiliko ya mfumo wa malipo ya kidijitali.

Aidha, uhamasishaji wa zoezi hilo umefanywa na Mrajis Msaidizi wa Mkoa wa Tabora, Peja Mhoja pamoja na Mrajis Msaidizi (Uhamasishaji), Ibrahim Kadudu, ambao wamekuwa mstari wa mbele kuwahamasisha wakulima kujiunga na mifumo rasmi ya kifedha ili kunufaika na malipo ya kisasa, salama na yenye tija.

Na Janeth Raphael MichuziTv


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amezitaka taasisi za kifedha nchini kubadili mtazamo katika utoaji wa mikopo kwa kuweka mkazo zaidi kwenye uaminifu, historia ya biashara na mwenendo wa miamala ya waombaji, badala ya kutegemea dhamana za mali zinazoonekana pekee.

Akizungumza leo Juni 12, 2026 katika maadhimisho ya miaka 60 ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam, Rais Samia alisema wanawake na vijana wengi wamekuwa wakikosa fursa za kifedha licha ya kuwa na biashara zenye mafanikio na uwezo wa kurejesha mikopo.

Ameeleza kuwa sehemu kubwa ya wanawake na vijana hawamiliki mali kama nyumba, viwanja au magari vinavyoweza kutumika kama dhamana, jambo ambalo limeendelea kuwa kikwazo katika kupata huduma za mikopo kutoka taasisi mbalimbali za fedha.

Rais Samia amesema makundi hayo yana rekodi nzuri za biashara, mauzo yanayoonekana na historia ya miamala inayothibitisha uwezo wao wa kuendesha shughuli za kiuchumi kwa mafanikio, hivyo yanastahili kupewa nafasi zaidi ya kupata mitaji.

Amezitaka benki na taasisi nyingine za kifedha kubuni mifumo ya kisasa itakayowezesha kutathmini uwezo wa wakopaji kwa kutumia taarifa za biashara na mwenendo wao wa kifedha ili kuongeza ushiriki wa wanawake na vijana katika uchumi.

Aidha, Rais Samia amesisitiza kuwa uaminifu wa mteja ni rasilimali muhimu inayopaswa kupewa uzito mkubwa katika maamuzi ya utoaji wa mikopo, akionya dhidi ya kuwanyima wananchi fursa kwa sababu ya kutokuwa na mali zinazokubalika kama dhamana za kawaida.

Katika hatua nyingine, amezitaka taasisi za kifedha kuongeza uwazi kwa kuwapatia wananchi taarifa sahihi na za kueleweka kuhusu masharti ya mikopo kabla ya kuingia kwenye mikataba ya ukopaji.

Amesema ni muhimu kwa wakopaji kuelewa kiwango halisi cha mkopo, muda wa marejesho, viwango vya riba na gharama nyingine zote zinazohusiana na mkopo huo ili waweze kufanya maamuzi sahihi ya kifedha.

Rais Samia pia ameeleza kuwa mafanikio ya sekta ya fedha hayapaswi kupimwa kwa idadi ya watu waliounganishwa kwenye huduma za kifedha pekee, bali kwa kiwango ambacho huduma hizo zinachochea ukuaji wa biashara, kuongeza mitaji na kuboresha maisha ya wananchi.

Kauli hiyo inakuja wakati Serikali ikiendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuimarisha ushiriki wa wananchi katika shughuli za kiuchumi na kuweka mazingira bora yatakayowezesha sekta binafsi kuchangia kwa kiwango kikubwa zaidi katika maendeleo ya taifa.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akikagua mabanda ya maonesho katika Maadhimisho ya miaka 60 ya Benki Kuu ya Tanzania yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Jijini Dar es Salaam tarehe 12 Juni, 2026.

Na Janeth Raphael MichuziTv

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ameielekeza Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kuongeza uwezo wa kuchambua na kutambua mapema mwelekeo wa uchumi wa ndani na wa kimataifa ili kusaidia taifa kukabiliana na changamoto pamoja na kunufaika na fursa zinazojitokeza katika mazingira ya uchumi wa dunia yanayobadilika kwa kasi.

Akizungumza katika maadhimisho ya miaka 60 ya Benki Kuu ya Tanzania yaliyofanyika jijini Dar es Salaam leo Juni 12, 2026, Rais Samia alisema dunia inaendelea kushuhudia misukosuko ya kisiasa, kiuchumi na kifedha ambayo imekuwa na athari kubwa kwa upatikanaji wa bidhaa, uthabiti wa masoko ya fedha pamoja na thamani ya sarafu katika mataifa mbalimbali.

Amesema kuwa mabadiliko hayo yamekuwa yakichochea kupanda kwa gharama za maisha, hususan kupitia ongezeko la bei za mafuta katika soko la dunia, hali inayosababisha kuongezeka kwa gharama za uzalishaji, usafirishaji na huduma mbalimbali.

Rais Samia amesema katika kipindi cha sasa, taasisi za fedha za taifa zinapaswa kwenda mbali zaidi ya jukumu la kawaida la kusimamia sera za fedha na kuhakikisha zinakuwa na mifumo madhubuti ya kutambua vihatarishi kabla havijageuka kuwa migogoro inayoweza kuathiri uchumi na ustawi wa wananchi.

Amesisitiza kuwa Benki Kuu inapaswa kujiimarisha katika ukusanyaji wa taarifa, uchambuzi wa takwimu na utabiri wa mwenendo wa uchumi ili iweze kutoa tahadhari za mapema na kusaidia serikali kufanya maamuzi sahihi kwa wakati.

“Katika mazingira ya sasa ya dunia, taasisi za fedha zinatakiwa kuwa na uwezo wa kuona mbele, kutambua mabadiliko yanayokuja na kuchukua hatua za mapema kulinda uchumi wa taifa,” alisema Rais Samia.

Katika hatua nyingine, Rais huyo ameeleza kuwa Tanzania imeendelea kuimarisha usalama wake wa kifedha kwa kutumia rasilimali za ndani, akitaja ongezeko la akiba ya dhahabu ya taifa iliyofikia tani 27.5 zenye thamani ya takribani Shilingi trilioni 10.

Amesema hatua hiyo ni sehemu ya mikakati ya kuimarisha uthabiti wa uchumi na kujenga kinga dhidi ya misukosuko ya kifedha inayoweza kujitokeza katika masoko ya kimataifa.

Rais Samia amebainisha kuwa mafanikio hayo yanaonyesha umuhimu wa kutumia rasilimali za ndani kama nyenzo ya kuimarisha uwezo wa taifa kukabiliana na changamoto za kiuchumi za sasa na zijazo.

Aidha Rais Samia amesema matarajio yake kwa Benki Kuu katika miaka ijayo, akitaka taasisi hiyo ijijenge kuwa chombo chenye uwezo wa kutambua kwa wakati hatari na fursa za kiuchumi kabla hazijaonekana wazi kwa wadau wengine.

Amesema lengo ni kuona BoT ikibadilika kutoka kuwa msimamizi wa mfumo wa fedha pekee na kuwa taasisi yenye mchango mkubwa katika kulinda mustakabali wa uchumi wa taifa kupitia uchambuzi wa kina, ubunifu na utabiri sahihi wa mwenendo wa uchumi.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea zawadi ya Kitabu cha picha za matoleo ya noti kuanzia mwaka 1966-2026, pamoja na Sarafu ya kumbukumbu ya miaka 60 ya Benki Kuu ya Tanzania kutoka kwa Gavana wa Benki hiyo Bw. Emmanuel Tutuba katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Jijini Dar es Salaam tarehe 12 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akihutubia viongozi pamoja na wageni mbalimbali waliohudhuria kwenye Maadhimisho ya miaka 60 ya Benki Kuu ya Tanzania katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Jijini Dar es Salaam tarehe 12 Juni, 2026.

 

Na Mwandishi Wetu

Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) imefanya mazungumzo na Kampuni ya Egyptian Holding Company for Silos and Storage (EHCSS) ya nchini Misri ili kuimarisha usimamizi wa ghala, matumizi ya teknolojia za kisasa na kukuza biashara ya bidhaa za kilimo kati ya Tanzania na Misri.

Mazungumzo hayo yamefanyika Juni 11, 2026 kati ya ujumbe wa WRRB ulioongozwa na Mkurugenzi Mtendaji, Asangye Bangu, akiongozana na Meneja wa Mipango Tafiti na Bunifu, Fidelis Temu na Afisa Ubora Anatolius Kabyemela na viongozi wa EHCSS wakiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu wa taasisi hiyo, Dkt.Ashraf Shedeq.

Katika kikao hicho, WRRB imeeleza uzoefu wa Tanzania katika utekelezaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala, huku EHCSS ikieleza namna inavyosimamia ghala za kisasa za kuhifadhi nafaka kwa kutumia teknolojia zinazosaidia kulinda ubora, usalama na ufanisi wa mazao.

Pamoja na hayo, Ujumbe wa WRRB pia umetembelea baadhi ya ghala za EHCSS na kujionea mifumo ya kisasa ya uhifadhi na usimamizi wa bidhaa.

Katika kuendeleza ushirikiano huo, taasisi hizo mbili zimekubaliana mambo kadhaa ikiwamo kuandaa makubaliano ya ushirikiano yatakayosaidia kuongeza fursa za bidhaa za Tanzania kuingia katika soko la Misri, kutoa mafunzo ya kitaalam kuhusu usimamizi wa ghala, kubadilishana uzoefu wa matumizi ya teknolojia za kisasa na kuwezesha biashara ndani ya soko la Afrika kupitia Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA).

Ushirikiano huo unatarajiwa kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya kimataifa na kufungua fursa mpya za biashara na uwekezaji kati ya nchi hizo mbili.


Top News