Na. Vero Ignatus,Arusha.

Serikali imepiga marufuku watumishi wa Uma Kutumia mitandao isiyo rasmi ambayo ni tofauti na ile iliyounganishwa na mfumo wa Serikali mtandao katika kutuma nyaraka na taarifa mbalimbali za serikali kwani si salama kwa usalama wa nchi na wananchi

 Marufuku hiyo imetolewa  l9 April 2026  na Waziri wa Nchi, Ofisi ya   Rais  Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Ridhiwani Kikwete wakati akifunga kikao kazi cha 6 cha serikali mtandao kilichofanyika kwa siku Tatu mkoani Arusha nakusema kwamba  watumishi wa Umma kutumia mifumo isiyo rasmi ni hatari kwani inasababisha nyaraka za siri za serikali kuonekana mtandaoni. 

Bado tunao wafanyakazi wa Serikali wanatumia Mtandao binafsi kurusha taarifa za Serikali jambo ambalo siyo sawa kwa taarifa hizo za Serikali kuwekwa wazi jambo hilo liwe narufuku kuanzia Leo taarifa za Serikali kutumwa kwa Mtandao binafsi. Alisema

Kikao Kazi hicho  cha siku tatu, kimewakutanisha takribani washiriki 1,000 kutoka sekta za umma na binafsi, na kimejadili kwa kina masuala muhimu yanayohusu ujenzi, uendelezaji na usimamizi wa jitihada za Serikali Mtandao. Ambapo Kupitia mijadala hiyo wamepata fursa ya: Kutathmini utekelezaji wa maazimio ya Kikao Kazi kilichopita,, Kubainisha mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa miradi ya TEHAMA Serikalini,

Pia waliweza Kujadili changamoto zilizopo na kuweka mikakati ya pamoja ya kukabiliana nazo,Na kuweka maazimio mapya yatakayotuongoza katika hatua zinazofuata za kuendelea kuboresha utendaji kazi na utoaji wa huduma za umma kwa njia ya kidijitali.

Kikwete amesema amefarijika kuona kuwa, mijadala yote imejikita katika uzingatiaji wa Sheria, Kanuni,Viwango na Miongozo ya Serikali Mtandao, jambo ambalo ni msingi muhimu wa kuhakikisha miradi ya TEHAMA Serikalini inakuwa salama, endelevu na yenye kujali Katika kikao kazi hiki, 

Sambamba na hayo Serikali kupitia Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA), itatoa tuzo kwa taasisi zilizofanya vizuri katika kuzingatia Sheria, Kanuni, Viwango na Miongozo ya Serikali Mtandao, kwenye utekelezajiwa miradi ya TEHAMA.ambapo  amezipongeza taasisi zote zilizotunukiwa tuzo hizo  na kusema Tuzo hizo si za heshima tu, bali ni chachu ya kuhamasisha ubora, uwajibikaji na uzingatiaji wa misingi ya Serikali Mtandao katika taasisi zote za umma.



Na Mwandishi Wetu
KAMPUNI ya Kitanzania ya Compact Energies, inayojihusisha na uzalishaji na usambazaji wa vifaa vya kisasa vinavyotumia nishati ya jua, imesema kuwa Tanzania ina nafasi kubwa ya kuleta mageuzi ya kiuchumi kupitia uwekezaji katika teknolojia za uzalishaji wa umeme wa jua kwa matumizi ya majumbani na viwandani.

Akizungumza wakati wa Mkutano wa 5 wa Z-Summit Zanzibar uliomalizika hivi karibuni Visiwani Zanzibar, Meneja wa Masoko na Mauzo wa kampuni hiyo, Bw. Joseph Madata Biseko , alisema kuwa uwekezaji katika uzalishaji wa nishati ya jua utasaidia kupunguza gharama za uzalishaji viwandani na hivyo kuchochea ukuaji wa uchumi.

Aliongeza kuwa matumizi ya nishati ya jua yatasaidia pia kupunguza gharama za maisha kwa wananchi, kwa kuwa ni nishati nafuu na inayopatikana kwa uhakika ikilinganishwa na vyanzo vingine vya umeme vyenye gharama kubwa .

“Uzuri wa umeme wa jua, gharama ni wakati wa kuunganisha tu na hakuna malipo ya mwezi, ukitofautisha na aina nyingine ya nishati,”

“Kampuni yetu imejipanga kutoa suluhisho la changamoto za upatikanaji wa umeme usio wa uhakika kwa kusambaza vifaa vya ubora wa hali ya juu kwa gharama nafuu, ili Watanzania na wawekezaji wa kigeni wanufaike kupitia uzalishaji wa bidhaa na utoaji wa huduma mbalimbali,” amesema Bw. Biseko

Mkutano huo uliwakutanisha wadau mbalimbali kutoka sekta za utalii, uuzaji wa viwanja na nyumba, pamoja na nishati. Washiriki walitoka katika nchi mbalimbali zikiwemo Kenya, Uganda, Ghana, Nigeria, Tanzania Bara na Zanzibar.

Kupitia jukwaa hilo, kampuni hiyo, iliyoshinda tuzo ya ‘Africa Company of the Year Awards’ katika kipengele cha Makampuni Makubwa Barani Afrika kutoka nchi 26 mwaka 2024, pia ilipata fursa ya kuonesha bidhaa na huduma zake, huku ikisisitiza umuhimu wa uwekezaji katika nishati jadidifu kama msingi wa maendeleo endelevu ya kiuchumi nchini.



*Atambulisha jukumu jipya la Mahusiano linaloratibiwa na Wizara Yake.

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Clement Sangu (Mb.) ametembelea Ofisi za Jumuiya ya Maridhiano na Amani Tanzania (JMAT) Makao Makuu Februari 19 2026 Jijini Dar es Salaam na kukutana na Viongozi kwa lengo la kujitambulisha na kulitambulisha jukumu jipya la Mahusiano ambalo Ofisi yake imekabidhiwa kuliratibu.

Aidha, Waziri Sangu alipowasili amepokelewa na
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maridhiano na Amani Tanzania (JMAT ) Dkt. Alhad Mussa Salum pamoja na wajumbe wa jumuiya hio.

Akizungumza katika kikao hicho, Waziri Sangu alipongeza Jumuiya hiyo kwa mchango wake mkubwa katika kuimarisha amani, umoja na mshikamano nchini kupitia Maridhiano.

Vilevile, alieleza kuwa JMAT imekuwa nguzo muhimu ya maadili na mshikamano wa kijamii kwa kuhimiza maridhiano ya amani, kuvumiliana na kuimarisha mahusiano mema baina ya waumini wa dini mbalimbali.

"Juhudi hizo zimechangia kwa kiasi kikubwa kudumisha utulivu na mshikamano wa kitaifa" amesema Mhe. Sangu.

Aidha, Mhe. Sangu amesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Serikali na taasisi za kidini katika kushughulikia changamoto za kijamii, kiuchumi, kisiasa, kikanda na kimataifa hususan malezi bora na maadili mema katika jamii.

Sambamba na hayo, ameihakikishia JMAT kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan itaendelea kushirikiana na Baraza hilo na taasisi mbalimbali kuendeleza agenda ya amani, mshikamano na maendeleo jumuishi.

Kwa upande wake Mwenyekiti Jumuiya ya Maridhiano na Amani Tanzania (JMAT) Dkt. Alhad Mussa Salum, amempongeza Rais kwa kutambua umuhimu wa Mahusiano na kuanzisha Wizara mahsusi inayoshughulikia mahusiano.

Aidha, ameishukuru Serikali kwa kutambua na kuthamini mchango wa Jumuiya na kuahidi kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuimarisha umoja wa kitaifa, amani na mshikamano.
Mkutano wa 6 wa Serikali Mtandao umemalizika Februari 19, 2026, huku Halmashauri ya Wilaya ya Geita ikitangazwa kuwa Mshindi Namba Moja kati ya Halmashauri 184 nchini katika matumizi bora ya mifumo ya kiserikali kwa kuzingatia sheria, viwango na miongozo inayotolewa na Mamlaka ya Serikali Mtandao.

Tuzo hiyo imetolewa katika Mkutano wa 6 wa Serikali Mtandao uliofanyika katika ukumbi wa Arusha International Conference Centre (AICC), jijini Arusha na kukabidhiwa na Mhe Ridhiwani Kikwete, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wakati akifungua Kikao hicho cha 6.

Mkutano huo wa siku 3, ulifunguliwa rasmi Februari 17, 2026 na Mhe Moses Mpogole Kusiluka, Katibu Mkuu Kiongozi (KMK) ambapo amesema Nchi ya Tanzania ipo katika muelekeo sahihi wa mageuzi ya kidijitali. "Mimi naiona Tanzania nzuri sana wala sio baadaye sana ni hivi Karibuni" Amesema Balozi Dkt Kusiluka.

Vile Vile Katibu Mkuu Kiongozi amesema Serikali imewekeza kwa kiasi kikubwa kwenye TEHAMA na hii ni kwa kutambua kuwa maendeleo ya sasa hayawezi kupatikana nje ya mifumo ya kidijitali.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri, Karia Magaro, ameishukuru Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGa) kwa kutambua juhudi hizo, na amekipongeza Kitengo cha TEHAMA kwa usimamizi madhubuti wa mifumo ya kiserikali inayowezesha utoaji wa huduma bora kwa wananchi.

"Tuendelee kujikita kwenye mifumo na kuongeza kasi katika mifumo yote inayoletwa na Serikali" Amesema Magaro.

Naye Mkuu wa Kitengo Cha TEHAMA, Halmashauri ya Wilaya ya Geita Frank Makonda ametoa rai kwa watumishi wa Halmashauri kuendelea kushirikiana na kuongeza bidii kwenye ubunifu wa kutoa huduma kwa wananchi kwa kufuata Sheria na miongozo inayotolewa na Mamlaka ya Serikali Mtandao.

Ushindi Huo wa Tuzo hiyo (Best Performance in Compliance to e-Government Act, Standards and Guidelines) ni ushahidi kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Geita chini ya Mkurugenzi Mtendaji Karia Rajab Magaro, inaongoza kwa ubunifu, uwazi na matumizi sahihi ya TEHAMA katika utumishi wa umma.

Kikao hicho kimeongozwa na Kauli Mbiu isemayo " Kuboresha utendaji wa Serikali kwa kuimarisha utoaji wa huduma za umma kupitia mifumo salama na Jumuishi ya Serikali Mtandao.







Leo tarehe 20.2.2025 Mkuu wa mkoa wa Rukwa. Mhe. Makongoro Nyerere ametembelea Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) na kuwasilisha pongezi zake kuwa Tangu kuanzishwa kwake TADB ni benk ambayo imekuwa kwa kasi kubwa ndani ya miaka kumi (10) ikihudumua wakulima, wafugajo na wavuvi ambao mkoani Rukwa wapo na wanategemea mikopo ya benki hii kwa masharti ya riba nafuu.

Akipokea ugeni huo Bw. Frank Nyabundege Amempongeza Mhe. RC kwa kuaminiwa na kuteuliwa na Mhe Rais kuwa mkuu wa mkoa wa Rukwa.

Aidha amemuelezea kuwa mafanikio ya Benk ya TADB yametokana na jitihada za Serikali awamu ya sita inayoongozwa na Mhe.Dkt Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania kuiongezea benk fedha katika mtaji wa benki ili kufikia wakulima, wafugaji na wavuvi wengi hapa nchini.


Leo tarehe 20.2.2026 Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo ya kilimo Tanzania (TADB) Bw. Frenk Nyabundege amepokea ujumbe wa TANZANIA NATIONAL CHAMBER OF COMMERCE ukiongozwa na Bw.Painetho Madembwe akiambatana na wawakilishi toka TNCC makao makuu pamoja na AGGOT waliotembelea katika ofisi za TADB makao makuu kinondoni jijini dar es salaa.

Lengo la ugeni huo ni kukabidhi Tuzo ya shukrani kwa TADB kufanikisha na kuchagiza maendeleo ya biashara za kilimo mkoani iringa Na kuwezesha Mikopo yenye kusaidia ustawi wa kilimo cha chai, kahawa,parachichi na mahindi huko kilolo mkoani iringa.

Akipokea tuzo hiyo Bw. Nyabundege amewahakikishia kuwa benki yao itaendelea kutoa huduma za kifedha kwa wakulima na wafugaji katika mikoa yote na kuchagiza kilimo kuleta mtazamo wa kilimo biashara ambacho kinabenkika kwa maslahi ya ustawi wa wakulima na uchumi wa nchi.




Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Jakaya Kikwete, ameweka jiwe la msingi la ujenzi wa chuo cha Utumishi wa Umma Kampasi ya Tanga, leo tarehe 20 Februari 2026. 

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mheshimiwa Kikwete amethibitisha kuwa serikali imeamua kutumia kiasi cha shilingi bilioni 39 kwa ajili ya ujenzi wa kampasi hiyo, fedha zitakazotengwa kila mwaka hadi kukamilika kwa mradi mzima.
 
 “Namshukuru sana Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samaia Suluhu Hassan kwa kukubali na kuruhusu kutenga kiasi cha shilingi Bill 39 za ujenzi wa Kampasi ya Tanga” amesema Mhe. Kikwete. 
Aidha, amesisitiza ujenzi wa mradi wa kampasi ya Tanga unatokana na elimu kuwa kipaumbele na kusisitiza kuwa serikali   itaendelea kuwekeza katika elimu na kuhakikisha utumishi wa umma unaboreshwa nchini ambalo ni jukumu la chuo kuwajengea uwezo watumishi wa umma nchini.

Pia Mhe. Kikwete amesema kuwa, ameridhishwa na kiwango cha kazi kilichofanyika na kuipongeza menejimenti ya chuo kwa kusimamia kwa makini ujenzi wa kampasi. Amesema kuwa ujenzi huu unalenga kuimarisha huduma za utumishi wa umma nchini kupitia kampasi itakayojenga mustakabali mzuri wa elimu na utumishi bora.

    Akitoa taarifa ya mradi wa ujenzi, Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, Dkt. Ernest Mabonesho amesema kuwa awamu ya kwanza ya ujenzi ilianza rasmi tarehe 8 Februari 2025, ikiwa ni ujenzi wa jengo la ghorofa mbili la  madarasa gharama za takriban shilingi bilioni 6.16. 

Dkt. Mabonesho amesema kua, Jengo litajumuisha madarasa 26 yatakayohudumia zaidi ya wanafunzi 2,500 kwa awamu moja, ofisi 24 za watumishi, kumbi mbili za mikutano, na vyoo vya kisasa 18. Vilevile, amesema jengo hili litakuwa na miundombinu ya kisasa ya TEHAMA itakayowezesha matumizi ya teknolojia katika kufundisha, kujifunza, na kuendesha shughuli za kitaaluma kwa ufanisi zaidi.

Dkt. Mabonesho pia alibainisha kuwa mradi huu utaleta manufaa makubwa kwa wananchi kiuchumi kutokana na huduma zitakazotolewa na chuo, ikiwemo kuimarisha ajira na maendeleo ya kijamii. Ujenzi huu unaonyesha dhamira ya serikali ya kuimarisha sekta ya elimu na utumishi wa umma nchini, na kuleta maendeleo zaidi kwa mkoa wa Tanga na taifa kwa ujumla.

Mradi wa ujenzi wa Kaampasi ya Tanga unatekelezwa katika eneo la hekari 14 lililopo Kange Uzunguni, mjini Tanga. Awamu ya kwanza ya ujenzi ilianza rasmi tarehe 8 Februari 2025,













 

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amekutana na kufanya mazugumzo na Balozi wa India nchini Tanzania Mhe. Bashwadip Dey, mazungumzo yaliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 20 Februari 2026.

Mazungumzo hayo, yamelenga kuimarisha zaidi ushirikiano baina ya India na Tanzania katika sekta mbalimbali za kimkakati. Mahusiano kati ya nchi hizi mbili yamejikita katika sekta ya Afya, Maji, Elimu,Biashara na Uwekezaji pamoja masuala ya Ulinzi na Usalama.

Tanzania na India zina mahusiano mazuri ya kidiplomasia yaliyoanza baada ya Tanzania kupata uhuru ambapo India ilifungua Ubaozi wake mwaka 1961 na Tanzania kufungua Ubalozi wake nchini India mwaka 1962.

Mwaka 2023 mahusiano kati ya nchi hizi mbili yaliongezeka zaidi na kuwa mahusiano ya kimkakati kufuatia ziara rasmi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, aliyoifanya nchini India.

India imekuwa na mchango mkubwa katika miradi mbalimbali ya maji inayotekelezwa na Serikali pamoja na kutoa mchango mkubwa katika sekta ya Afya ikiwemo utoaji wa huduma za afya nchini, mafunzo pamoja na Vifaa Tiba.

India imekuwa mdau muhimu wa biashara nchini Tanzania ambapo hadi sasa inashika nafasi ya tatu duniani kwa kufanya biashara na Tanzania. Bidhaa ambazo Tanzania inauza zaidi nchini India ni pamoja na Korosho, karanga, mboga za jamii ya kunde, vito vya thamani na vito vya thamani, pamba; karafuu, chai, Ngozi, mbao na bidhaa za mbao.









Na Mwandishi Wetu

Watumiaji wa gesi ya kupikia wamepata nafuu baada ya Oryx Gas Tanzania kuzindua kampeni ya “Pishi la Kibabe” kwa Ramadhan na Kwaresma, itakayoshusha bei ya mtungi mpya wa kilo sita hadi Sh. 37,000 nchi nzima.

Akizungumza leo Februari 20,2026 jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi huo Meneja Masoko na Mauzo wa Oryx Gas Tanzania Shaban Fundi amesema huu ni mwezi wa kujitafakari ,kushirikiana ,kujitolea na zaidi ya yote kuunganisha watu wote.

“Ili kuunga mkono wateja wetu katika kipindi hiki maalum tunatoa bei ya promosheni kwenye mitungi yetu mipya ya kilo sita itauzwa kwa Sh.37000 nchi nzima hadi Zanzibar.”amesema Fundi

Pia amesema mbali ya kupunguza bei katika kipindi hiki cha Ramadhan na Kwaresma wateja wao watakaonunua au kujaza gesi kwenye maduka maalum ya Oryx na Mangi Shop watapokea zawadi ya futari papo kama ishara ya shukrani yao kwao.

Akizungumza kuhusu gharama za mtungi wa kilo sita amesema mpaka unafika nchini Tanzania gharama yake haipungui Sh.80,000 lakini Oryx katika soko mtungi huo unapatikana kwa Sh.40000 na kwa sasa tumetoa promosheni mpaka Sh.37000.

-“Hata hivyo tunaomba Serikali iendelee kuangalia katika maeneo mengine ili kuhakikisha kwamba gesi pamoja na mtungi bei yake inakuwa chini ili wananchi waweze kupata kwa bei nafuu.Kwafanya hivyo Oryx Gas kwa kushirikiana na Serikali tunaweza kufanikisha matumizi ya nishati safi kwa wananchi wengi zaidi.”

“Kuhusu gharama ukilinganisha mkaa na kuni bei yake iko juu zaidi ya nishati safi ya kupikia kwani kwa familia ya kawaida kwa siku moja inatumia kopo moja la mkaa ambalo linauzwa Sh.2000 hivyo kwa mwezi ni Sh.60,000 wakati mtungi wa gesi ya oryx wa kilo 6 ni Sh.40,000.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Oryx Gas Tanzania Benoit Araman amesema lengo la kampeni iliyozinduliwa kwa ajili ya Mfungo wa Mwezi wq Ramadhan na Kwaresma ni muendelezo wa kuhamasisha matumizi ya nishati safi nchini ikiwa ni kuunga mkono juhudi za Serikali za kuhimiza wananchi kutumia nishati safi ya kupikia.

“Oryx Gas lengo letu kubwa ni kuendelea kuhamasisha nishati safi ya kupikia na mimi na timu yangu tumejipanga vema kuhakikisha tunaendelea kufanya kampeni za kuwezesha wananchi kutumia nishati safi ya kupikia.Wakati huu wa Ramadhan na Kwaresma tunawatakia mfungo mwema lakini wakati huo huo tukihamasisha matumizi ya nishati safi.”

Wakati huo huo Mkuu wa Idara ya Mauzo ya Gesi kwa Ujumla Carloline Msokwa amesema kipindi hiki Waislamu na Wakristo wanaungana pamoja kuomba toba na ni kipindi ambacho familia zinakaa kufanya ibada na kuomba toba lakini pia ni wakati wa kupika chakula kizuri kwa ajili ya kufuturu.

“Kwahiyo Oryx Gas tumekuja na kampeni ya Pishi la kibabe ambapo familia zitakaa na kupika pamoja lakini pia Oryx tumetoa punguzo la bei ili kuwezesha wananchi kutumia gesi.Pia nitoe rai huu ni wakati wa Watanzania kuwa wamoja na tuliombee taifa letu.”





Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Kanda ya Kati, Dodoma, Dkt. Japhet Nkangaga (kushoto), akipokea changamoto mbalimbali zinazowakabili wafugaji kutoka kwa muuzaji wa pembejeo za mifugo Manispaa ya Singida, Bi. Ester Munuo, tarehe 19 Februari 2026 mkoani Singida, wakati wa ziara ya uhamasishaji kwa wauzaji wa pembejeo za mifugo iliyolenga kutoa elimu kuhusu matumizi sahihi ya chanjo ya Matone (TEMEVAC) na taratibu za upatikanaji wa leseni za uuzaji wa viuatilifu vya rejareja na jumla.


*************


Na Daudi Nyingo – Singida

Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) imeendelea kuimarisha juhudi za kulinda afya ya mifugo nchini kwa kutoa elimu kwa wauzaji wa pembejeo za mifugo mkoani Singida kuhusu utoaji na matumizi sahihi ya chanjo za mifugo zinazozalishwa na taasisi hiyo. 

Zoezi hilo lililofanyika tarehe 19 na 20 Februari 2026 lililenga kuwajengea uwezo wauzaji wa pembejeo kama kiungo muhimu cha kuwafikia wafugaji, ili waweze kutoa elimu sahihi kuhusu utambuzi wa chanjo za TVLA, namna bora ya kuzitunza, matumizi sahihi na umuhimu wa kufuata taratibu za kitaalamu katika utoaji wa chanjo.

Akizungumza wakati wa kuhitimisha zoezi hilo tarehe 20 Februari 2026, Meneja wa TVLA Kanda ya Kati Dodoma, Dkt. Japhet Nkangaga, alisema kuwa ziara hiyo ililenga kutoa elimu kwa wauzaji wa pembejeo na wafugaji kuhusu matumizi sahihi ya chanjo ya Matone (TEMEVAC), ikiwemo namna bora ya kuzipokea, kuzihifadhi katika ubaridi unaostahili ili kudumisha ubora wake na kuhakikisha chanjo zinatumika kwa ufanisi unaokusudiwa.

“Tunasisitiza matumizi sahihi kuanzia hatua ya kufungua chupa ya chanjo. Kama imeandikwa kuwa na dozi 100, ni lazima itoe dozi 100. Endapo tundu litatobolewa kubwa, kunakuwa na uwezekano wa chanjo kutoka nyingi zaidi na kusababisha dozi zilizokusudiwa kutotimia,” alisema Dkt. Nkangaga.

Aliongeza kuwa elimu hiyo pia inahusisha matumizi sahihi ya chanjo baada ya kufunguliwa, akieleza kuwa kuku mmoja hupatiwa tone moja la chanjo na kurudiwa kuchanjwa baada ya miezi mitatu, utaratibu unaoendelea kwa mwaka mzima hadi kuku anapofikia hatua ya matumizi ya binadamu.

Baadhi ya wauzaji wa pembejeo za mifugo mkoani Singida wameibua changamoto ya upatikanaji wa chanjo mbalimbali, hali ambayo imekuwa ikiwalazimu wakati mwingine kupata chanjo kutoka vyanzo visivyo na uhakika. Wameshauri TVLA kuimarisha upatikanaji wa chanjo ili kuhakikisha wauzaji na wafugaji wanapata bidhaa salama, zenye ubora na kutoka katika vyanzo vinavyoaminika, hatua itakayosaidia kudhibiti tatizo la chanjo zisizo halali sokoni.

Bi. Ester Munuo, muuzaji wa pembejeo za mifugo mkoani humo, alisema kuwa pamoja na chanjo ya Newcastle (TEMEVAC), kuna umuhimu wa TVLA kuongeza uzalishaji wa aina nyingine za chanjo za kuku, zikiwemo chanjo za gumboro na ndui, ili kuwapa wauzaji uhakika wa chanzo sahihi cha chanjo.

“Tunapopata chanjo kutoka mamlaka moja inayoaminika, inatusaidia kuepuka kuchukua chanjo kutoka vyanzo visivyo na uhakika, jambo ambalo linaweza kuleta changamoto kwa mtumiaji na kuathiri imani ya wafugaji,” alisema.

Kwa upande wake, Bw. Anthony Ntobi alisema kuwa upatikanaji wa chanjo kwa wakati na kupitia mamlaka rasmi utarahisisha kazi ya wauzaji na kuongeza ufanisi kwa wafugaji.

“Kuna baadhi ya chanjo za kuku ambazo wakati mwingine husambazwa kwa nyakati tofauti. Kupata chanjo moja kwa moja kutoka mamlaka husika kutarahisisha upatikanaji, kupunguza hatari ya chanjo feki na kutuwezesha kuwahudumia wafugaji kwa ufanisi zaidi,” alisema.

TVLA imeeleza kuwa itaendelea kutoa elimu kwa umma na wadau wa sekta ya mifugo katika mikoa mbalimbali nchini kama sehemu ya mkakati endelevu wa kitaifa wa kuimarisha afya za mifugo, kuongeza uzalishaji na kuchangia maendeleo ya sekta ya mifugo nchini.
Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Kanda ya Kati, Dodoma, Dkt. Japhet Nkangaga (kushoto), akitoa elimu kwa muuzaji wa pembejeo za mifugo Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni, Bi. Stella Kahimba, kuhusu taratibu za upatikanaji wa leseni za uuzaji wa viuatilifu vya rejareja na jumla, wakati wa ziara ya uhamasishaji kwa wauzaji wa pembejeo za mifugo iliyofanyika tarehe 20 Februari 2026 mkoani Singida.
Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Kanda ya Kati, Dodoma, Dkt. Japhet Nkangaga (wa pili kutoka kulia), akitoa elimu kwa muuzaji wa pembejeo za mifugo Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni, Bi. Zainabu Ayubu (wa pili kutoka kushoto), kuhusu matumizi sahihi ya chanjo ya Matone (TEMEVAC), ikiwemo namna bora ya kuzipokea, kuzihifadhi na kuzitumia kwa ufanisi, wakati wa ziara ya uhamasishaji iliyofanyika tarehe 20 Februari 2026 mkoani Singida. Wa kwanza kushoto ni Bw. Charles Wambula Afisa Mifugo Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni.
Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Kanda ya Kati, Dodoma, Dkt. Japhet Nkangaga (kulia), akitoa elimu kwa muuzaji wa pembejeo za mifugo Halmashauri ya Wilaya ya Itigi, Bi. Dorcus Sumary, kuhusu matumizi sahihi ya chanjo ya Matone (TEMEVAC) pamoja na taratibu za upatikanaji wa leseni za uuzaji wa viuatilifu vya rejareja na jumla, wakati wa ziara ya uhamasishaji iliyofanyika tarehe 20 Februari 2026 mkoani Singida.
Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Kanda ya Kati, Dodoma, Dkt. Japhet Nkangaga (katikati), akitoa elimu kwa muuzaji wa pembejeo za mifugo Halmashauri ya Wilaya ya Itigi, Bw. Sifael Marko (kushoto), kuhusu matumizi sahihi ya chanjo ya Matone (TEMEVAC) pamoja na taratibu za upatikanaji wa leseni za uuzaji wa viuatilifu vya rejareja na jumla, wakati wa ziara ya uhamasishaji iliyofanyika tarehe 20 Februari 2026 mkoani Singida.

Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Kanda ya Kati, Dodoma, Dkt. Japhet Nkangaga, akitoa elimu kwa muuzaji wa pembejeo za mifugo Manispaa ya Singida, Bw. Abeid Hassan, kuhusu taratibu za upatikanaji wa leseni za uuzaji wa viuatilifu vya rejareja na jumla, wakati wa ziara ya uhamasishaji kwa wauzaji wa pembejeo za mifugo iliyofanyika tarehe 19 Februari 2026 mkoani Singida.

Top News