-Yatoa mwaka mmoja ili waweze kujiimarisha
WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali imetoa msamaha wa kodi ya mapato kwa kwa kipindi cha mwaka mmoja kwa wafanyabiashara wadogo ambao ni wapya ili waweze kujiimarisha katika biashara wanazozianzisha.
“Ili kuwavutia wajasiriamali, Serikali itatoa msamaha wa kodi ya mapato kwa wafanyabiashara wadogo ambao ni wapya kwa kipindi cha mwaka mmoja tangu tarehe ya kupata namba ya utambulisho wa mlipakodi,” amesema.
Amesema hatua hiyo itawawezesha akinamama lishe na baba lishe, waendesha bodaboda na bajaji, mafundi seremala na wachomeleaji na wengine wenye shughuli ndogondogo kuanzisha biashara zao bila kuwa na changamoto ya kudaiwa kodi ndani ya mwaka mmoja, na kwamba muda huo utatoa fursa ya kujiimarisha katika biashara wanazozianzisha.
Ametoa kauli hiyo bungeni jijini Dodoma leo (Ijumaa, Juni 26, 2026) wakati akielezea maeneo yaliyofanyiwa maboresho ya kodi katika hotuba ya kuhitimisha mkutano wa tatu wa Bunge. Bunge limeahirishwa hadi Agosti 25, mwaka huu.
Akielezea eneo jingine ambalo limewekewa nafuu ya kikodi, Waziri Mkuu amesema Serikali itasamehe kodi kwenye vifaa vitakavyotumika katika vituo vya kuchaji magari yanayotumia umeme na kupunguza ushuru wa forodha kutoka asilimia 25 hadi asilimia 10. Aidha, amewataka wadau wa sekta binafsi watumie fursa hiyo kuagiza mashine na vipuri vitakavyotumika kwenye vituo hivyo.
Akielezea azma ya Serikali kuimarisha mtiririko wa fedha katika mifuko ya miradi ya maendeleo, Dkt. Mwigulu amesema wa sasa asilimia 70 ya fedha za mifuko ya maendeleo zitaelekezwa moja kwa moja kwenye mifuko husika ili uweze kutekeleza majukumu yake ya kimsingi.
Amesema uamuzi huo utaongeza kasi na uhakika wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kupanua wigo wa huduma za jamii na kuongeza fursa za uzalishaji. Uamuzi huo unatokana na ushauri uliotolewa na Wabunge kwa Serikali wakiitaka ichukue hatua za haraka kuwezesha sekta mbalimbali ikiwemo maji, barabara na umeme zinapata fedha kwa wakati.
“Nitumie fursa hii kuwakumbusha watendaji wa taasisi ambazo zitapelekewa fedha hizo, wahakikishe wanakamilisha miradi iliyokusudiwa, tena kwa kuzingatia thamani ya fedha na miradi iwe na uimara. Wakumbuke kuwa dhamira na maelekezo ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kutekeleza kikamilifu miradi ya maendeleo kwa ajili ya ustawi wa Watanzania,” amesisitiza.
Akitoa mwelekeo wa bajeti na vipaumbele vya sekta kwa mwaka 2026/2027, Dkt. Mwigulu amesema vipaumbele vya kila wizara za kisekta vimezingatia maslahi mapana ya Taifa na kwamba bajeti ijayo itaendelea kuimarisha uwekezaji katika sekta za uzalishaji, miundombinu na huduma za jamii.
“Serikali imejipanga kuendelea kuimarisha mifumo ya mapato ya ndani na kupunguza utegemezi wa mikopo na misaada kutoka nje. Mkakati mmojawapo ni kupunguza utegemezi kutoka nje,” amesisitiza.
Amesema bajeti hiyo inaenda kuweka mazingira wezeshi ya kuvutia urasimishaji wa sekta isiyo rasmi ambayo inaajiri zaidi vijana na wanawake. Kupitia utaratibu mpya wa utoaji mikopo inayotokana na asilimia 10 ya mapato ya ndani ya halmashauri, Waziri Mkuu amezielekeza taasisi za fedha na waratibu wa mikopo hiyo kuondoa masharti magumu yanayokwamisha wajasiriamali kunufaika na mikopo hiyo.
“Mfano ni ulazima wa wahitaji kwa upande wa watu wenye ulemavu kutakiwa kuunda vikundi na ulazima wa wahitaji kuwasilisha dhamana kubwa kama vile hati za nyumba ambavyo kwa asili ya biashara zao, hawawezi kuwa navyo,” amesisitiza.
Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Angellah Jasmine Kairuki (Mb) afungua kikao cha majadiliano kuhusu DPI for Inclusive Growth katika Wiki ya Kimataifa ya Teknolojia Huria (UN Open Source Week 2026) jijini New York, Marekani.
Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizoandaa maadhimisho hayo yanayohudhuriwa na mataifa na wadau mbalimbali wa teknolojia ulimwenguni.
Katika hotuba yake ya ufunguzi Waziri Kairuki alisema Tanzania imepiga hatua katika ujenzi wa mifumo ya kidijitali ikiwemo utambuzi wa kidijitali, mifumo ya malipo na mifumo ya kubadilishana taarifa kati ya sekta mbalimbali, ambayo ni msingi wa mageuzi ya kidijitali na utoaji wa huduma bora kwa wananchi.
Waziri Kairuki amesema Serikali chini ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuimarisha miundombinu ya kidijitali kupitia Mkongo wa Taifa wenye zaidi ya kilomita 27,000 za nyuzi za mawasiliano, vituo vya kuhifadhi data na mifumo inayounganisha taasisi za umma na binafsi.
Aidha, amesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa katika matumizi ya teknolojia huria ili kuimarisha ubadilishanaji wa taarifa, usalama wa mtandao na matumizi salama ya Akili Unde (AI), akieleza kuwa hakuna nchi wala mwananchi anayepaswa kuachwa nyuma katika safari ya uchumi wa kidijitali.
.jpeg)
Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi amesema Watanzania wataanza kushuhudia kushuka kwa bei za mafuta kuanzia mwezi Julai mwaka huu kufuatia kuanza kushuka kwa bei ya mafuta ghafi katika soko la dunia baada ya kusitishwa kwa mapigano ya Mashariki ya Kati.
Akijibu mwongozo wa Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mhe. Subira Mgalu, Bungeni jijini Dodoma leo, Juni 26, 2026, Waziri Ndejembi amesema Serikali imezielekeza EWURA, TPDC na PBPA kuhakikisha manufaa ya kushuka kwa bei za mafuta katika soko la dunia yanawafikia walaji nchini.
Amesema licha ya athari za vita kati ya Iran, Israel na Marekani zilizosababisha usumbufu katika usafirishaji wa mafuta kupitia Mlango wa Hormuz, Tanzania iliendelea kuwa na uhakika wa upatikanaji wa mafuta bila kukumbwa na uhaba.
Ndejembi amesema hatua za haraka zilizochukuliwa na Serikali zilihakikisha mafuta yanapatikana katika maeneo yote ya nchi, huku Tanzania ikiendelea kuwa miongoni mwa nchi zenye bei nafuu za mafuta katika ukanda wa Afrika Mashariki.
Ameeleza kuwa baada ya makubaliano ya kusitisha mapigano, bei ya mafuta ghafi imeanza kushuka hadi kufikia takribani dola 70 kwa pipa, hali inayotarajiwa kuleta nafuu katika soko la ndani kadri shehena mpya zilizonunuliwa kwa bei ya chini zitakavyoingia nchini.
“Watanzania wataanza kuona punguzo la bei kuanzia mwezi Julai, na kadri shehena mpya za mafuta zilizonunuliwa kwa bei nafuu zitakavyoendelea kuwasili nchini, ndivyo bei zitakavyozidi kushuka,” amesema Waziri Ndejembi.
Aidha, amesema wataalamu wa soko la dunia wanatarajia ndani ya wiki nane hadi 10 bei za mafuta kurejea katika viwango vilivyokuwepo kabla ya kuanza kwa mgogoro huo mwezi Februari mwaka huu.
Waziri Ndejembi ameongeza kuwa Serikali itaendelea kufuatilia mwenendo wa soko la dunia huku ikiimarisha mikakati ya muda mrefu ya kuhakikisha upatikanaji wa mafuta nchini, ikiwemo kuongeza vyanzo vya uagizaji wa mafuta na kuharakisha utekelezaji wa mpango wa ujenzi wa kiwanda cha kusafisha mafuta mkoani Tanga ili kuimarisha usalama wa nishati nchini.
Mamlaka ya Majisafi na usafi wa Mazingira Tanga (Tanga UWASA) imepokea ugeni wa viongozi wa kanda na wawakilishi kutoka Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Maendeleo ya Mitaji (UNCDF) ukiongozwa na Katibu Mtendaji wa Mfuko huo Bw. Pradeep Kurukulasuriya uliolenga kutembelea na kujionea maendeleo ya utekelezaji wa Mradi wa kuboresha hali ya upatikanaji huduma ya maji Tanga awamu ya tatu kupitia ufadhili wa Hatifungani ya Kijani ambapo UNCDF ni miongoni mwa wadau muhimu walioshiriki katika hatua za awali za kufanikisha mradi huo.
Katika ziara hiyo, Katibu Mtendaji na wageni walipokea taarifa ya mradi na mwenendo wa magawio kwa wawekezaji pamoja na kutembelea eneo la mradi na kujionea kasi ya utekelezaji wa shuguli mbalimbali zinazolenga kuongeza na kuimarisha upatikanaji wa huduma ya maji ya uhakika kwa wakazi wa maeneo ya kihuduma ya Tanga UWASA unaotarajiwa kukamilika mapema mwezi Agosti, 2026.
Katibu Mtendaji pamoja na wageni walipata pia fursa ya kufanya kikao na sehemu ya wanufaika wa mradi wa Hatifungani katika Hospiali ya Jiji iliyopo kata ya Masiwani ambapo awali walikuwa wakipata changamoto katika kutoa huduma kutokana na adha ya upatikanaji wa huduma ya maji ya uhakika na kupitia mradi wa Hatifungani wameboreshewa miundombinu hivyo kuimarisha upatikanaji wa uhakika wa huduma ya majisafi.
Akizungumza mara baada ya ziara hiyo, Katibu Mtendaji wa UNCDF Bw. Pradeep Kurukulasuriya ameipongeza Tanga UWASA kwa uthubutu huo na kwa maendeleo mazuri ya utekelezaji wa mradi lengwa sambamba na kuonesha nia ya kuongeza wigo wa kuendelea kushirikiana.

" Tunajivunia kuwa sehemu ya mchango katika kufanikisha Hatifungani ya Kijani ya Tanga na matarajio yetu ni kwamba mradi huu utaboresha maisha ya jamii na kupitia hili Tanga UWASA imedhihirisha kuwa inawezekana kuhamasisha uwekezaji ndani ya nchi kwani takriban asilimia 65 ya uwekezaji ulitoka kwa wawekezaji wa Kitanzania, na kwa kupitia mpango huu, tumedhihirisha kuwa mitaji ya ndani inaweza kuhamasishwa ili kufadhili miradi muhimu ya maendeleo na kwa sasa tunasoma mfano huu kwa karibu, tunatafuta kuelewa ni nini kilifanya kazi vizuri, changamoto zipi zilizojitokeza, na ni somo gani tunaweza kujifunza ili tuweze kuiga mafanikio ya Hatifungani ya Tanga si tu ndani ya Tanzania bali katika nchi nyingine pia", alisema Bw. Kurukulasuriya.

Awali kabla ya ziara hiyo, Katibu Mtendaji wa UNCDF na wageni wakiongozwa na Kaimu Mkurugenzi wa Tanga UWASA, Eng. Salum Ngumbi walifika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tanga kutoa salamu na kupokelewa na Mkuu wa Wilaya ya Tanga Mhe. Dadi Kolimba aliyetoa salamu za Mkoa kwa niaba ya Mhe. Balozi Dkt. Batilda Salha Buriani Mkuu wa Mkoa wa Tanga
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Patrobas Katambi, amesema Tanzania inaendelea kuwa salama, tulivu na yenye amani, huku akionya kuwa Serikali haitamvumilia mtu yeyote atakayehusika na vitendo vya kuvuruga utulivu wa nchi kupitia mitandao ya kijamii au kwa njia nyingine yoyote.
Akizungumza Bungeni leo wakati akijibu swali la Mbunge wa Dodoma Mjini Paschal Chinyele aliyetaka kujua mambo yanayoendelea katika mitandao ya kijamii kuhusiana na Maandamano yanayoratibiwa na watu wasiojulikana na kuleta taharuki nchini je kama serikali suala hilo wanalifahamu na itachukua hatua gani kulinda usalama wa watanzania?
Katambi amesema ni kweli kumekuwa na baadhi ya watu wanaotumia mitandao ya kijamii kusambaza taarifa za upotoshaji, zenye uchochezi na zinazoweza kuzua taharuki kwa wananchi, jambo ambalo Serikali inalifuatilia kwa karibu.
Amesema Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi imepewa jukumu la msingi la kulinda amani na usalama wa nchi, hivyo hatua mbalimbali zinaendelea kuchukuliwa kuhakikisha hali hiyo inadumishwa wakati wote.
"Tumeanza kufuatilia viashiria vyote vya uvunjifu wa amani. Kila aliyepanga kuvuruga amani ya nchi kupitia mitandao ya kijamii au moja kwa moja katika jamii yetu atachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria," alisema Katambi.
Aidha, Waziri huyo amesema Serikali imekuwa ikishuhudia baadhi ya mikusanyiko ya watu ikitumika kutoa kauli na taarifa zinazoweza kuhatarisha amani ya nchi, hali ambayo haitavumiliwa.
Kutokana na hali hiyo, Katambi amemwelekeza Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) kutoa maelekezo kwa makamanda wote wa polisi kuanzia ngazi ya mikoa hadi kata kuimarisha mipango ya kiusalama katika maeneo yao.
Amesema ulinzi utaimarishwa kuanzia ngazi ya vitongoji hadi mitaa ili kuhakikisha usalama wa wananchi na mali zao unaendelea kuimarika katika kipindi chote.
Katambi pia amekumbusha kuwa hivi karibuni Tanzania itakuwa mwenyeji wa Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Sabasaba, yatakayohusisha wageni na wawekezaji kutoka mataifa mbalimbali, huku akisisitiza kuwa tukio hilo lina mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa nchi.
"Katika kipindi hiki chenye matukio muhimu ya kitaifa na hizi chokochoko zinazoendelea, hatutaweza kumvumilia mtu yeyote atakayefanya vurugu za aina yoyote. Ninawahakikishia wananchi waendelee na shughuli zao za kila siku kwa sababu vyombo vya usalama vimejipanga kikamilifu kudhibiti uhalifu na kuhakikisha nchi inaendelea kuwa salama," amesema.
Akizungumzia haki ya wananchi kutoa maoni yao, Katambi alisema Serikali ipo tayari kupokea hoja za msingi kupitia njia za mazungumzo badala ya maandamano au vitendo vya vurugu.
"Kama kuna hoja ya msingi, watu waje wazungumze nami. Nitasimama kama Serikali kupokea hoja hizo. Hadi sasa hakuna hoja yoyote ambayo Serikali imeshindwa kuitolea majibu," alisisitiza.
Mamlaka ya mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Pwani katika kuelekea kilele cha maadhimisho ya miaka 30 imeamua kurudisha fadhila kwa jamii pamoja na walipa kodi kwa kufanya usafi katika stendi ya mabasi chalinze pamoja na kutoa vifaa mbali mbali vya usafi kwa wafanyabiashara pamoja na kutoa vyombo mbali mbali vya kupikia kwa wakinamama ambao ni mama lishe.
Katika msafara huo ambao uliongozwa na Naibu Kamishna wa Mamlaka ya Mapato (TRA) Zanzibar Salehe Haji Pandu amesema kwamba wameamua kwenda kuwatembelea wafanyabiashara wa chalinze kwa lengo la kuweza kuwasaidia ili waweze kuhakikisha wanapiga hatua katika kutimiza ndoto zao.
"Katika kuelekea katika maadhimisho ya miaka 30 ya TRA tumeamua kwenda kufanya usafi katika stendi ya Chalinze ikiwa pamoja kugawa vifaa vya Usafi pamoja na Vyombo vya kupikia kwa Mama lishe pamoja na kuwawatembelea wafanyabiashara wa stendi ya Chalinze katika kutambua mchango wao kwa walipa kodi,"amebainisha Kamishna Haji.
Aidha Naibu Kamisha huyo amebainisha kwamba Mamlaka ya Mapato Tanzania kwa kiasi kikubwa inawategemea Wafanyabiashara hivyo ni muhimu kuhakikisha wafanyabiashara wanakua huku nguvu kubwa wakielekeza kwa wafanyabiashara walio nje ya wigo Kodi ili kuongeza idadi ya Walipakodi wengine Wapya.
Kwa upande wake Meneja wa TRA Mkoa wa Pwani Peter Eliona amessema kwamba wataendelea kushirikiana bega kwa bega na na wafanyabiashara wote na kuwahimiza kuweka misingi ya kuweza kulipa kodi kwa wakati kwa lengo la kuiwezesha serikali kupata mapato yao.
Meneja Eliona amebainisha kwamba wameona kuna umuhimu mkubwa wa kwenda katika stendi hiyo ya mabasi chalinz e na kupata fursa ya kuzungumza na wafanyabiashara ikiwa pamoja na kufanya matendoya kugawa mahitaji mbali mbali ambayo yatawasaidia katika suala zima la utekelezaji wa majukumu yao ikiwemo mama lishe pamoja na wafanyabiashara.
Naye Meneja wa Stendi ya Chalinze Henry Mwalugenge akizungumnza kwa niaba ya Mkurugenzi wa halmashauri ya Wilaya ya Chalinze amewashukuru TRA Mkoa wa Pwani kwa kutoa elimu ya Mlipakodi katika eneo hilo pamoja Vifaa vya Usafi ikiwani mojawapo ya kutengeneza mahusiano mazuri na Walipakodi.
Aidha Diwani wa Kata ya Bwilingu Laurence Peter amewapongeza TRA kwa kuvuka malengo ya ukusanyaji wa mapato na kurudisha kwa jamii itaongeza chachu ya Wafanyabishara kulipa kodi.
Akizungumnza kwa niaba ya Mama lishe Wa stendi ya mabasi chalinze,Mwenyekiti wa Mama lishe Bi.Zainabu Bakari amewashukuru TRA kwa kuwapa vifaa hivyo vitakavyo kwenda kuwarahisishia utendajikazi wao pamoja na kutengeneza mahusiano mazuri kwa walipa kodi.
Mamlaka ya mappato TRA Mkoa wa Pwani imeamua katika kuelekea maadhimisho ya miaka 30 imeamua kufanya mambo mbali mbali ikiwemo kufanya kongamano kwa walipa kodi na wadau, pamoja na kutembelea stendi ya mabasi chalinze na kugawa vifaa kwa wafanyabiashara, na mama lishe sambamba na kutoa elimu kwa mlipa kodi.
Dar es Salaam. Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu, amewataka waajiri nchini kutumia kikamilifu fursa ya msamaha wa tozo uliotolewa na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) kwa kulipa madeni ya michango ya wafanyakazi, akisisitiza kuwa hatua hiyo itapunguza gharama za uendeshaji, kuongeza uzalishaji na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.
Amesema msamaha huo ni sehemu ya juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuboresha mazingira ya biashara, kuimarisha mifumo ya hifadhi ya jamii na kusikiliza changamoto za waajiri ili kuongeza tija katika sekta binafsi na sekta ya ajira kwa ujumla.
Waziri Sangu alitoa wito huo jijini Dar es Salaam wakati wa Mkutano Mkuu wa 67 wa Chama cha Waajiri Tanzania (ATE), ambapo pia alishuhudia utiaji saini wa Hati ya Makubaliano (MoU) kati ya NSSF na ATE, yenye lengo la kuimarisha ushirikiano, kubadilishana taarifa na uzoefu, pamoja na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya taasisi hizo kwa manufaa ya waajiri, wafanyakazi na taifa.
Waziri Sangu alimpongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uongozi wake imara unaoendelea kuimarisha uchumi na kuboresha mazingira ya kazi nchini, akibainisha kuwa sekta ya ajira imeendelea kukua kutokana na sera madhubuti na ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Bw. Masha Mshomba, alisema msamaha huo ulioanza kutekelezwa Juni 1, 2026 hadi Desemba 31, 2026 unalenga kutoa unafuu kwa waajiri, kupunguza gharama na kuwawezesha zaidi katika uzalishaji.
Bw. Mshomba aliongeza kuwa ushirikiano kati ya NSSF na ATE utaimarisha utoaji wa elimu ya hifadhi ya jamii na kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa mifumo ya kinga ya kijamii kwa waajiri na wafanyakazi.
Naye, Mtendaji Mkuu wa Chama cha Waajiri Tanzania (ATE), Bi. Suzanne Ndomba-Doran, ameeleza kupongeza uamuzi wa NSSF wa kutoa msamaha wa adhabu na tozo, akisema hatua hiyo ni muhimu kwa waajiri kwani inawapa nafasi ya kurekebisha na kutimiza wajibu wao wa kisheria bila kuathiri kwa kiasi kikubwa uendelevu wa biashara zao. Alibainisha kuwa msamaha huo unaakisi ushirikiano wenye tija kati ya Serikali na taasisi za hifadhi ya jamii katika kuimarisha utii wa sheria, kuongeza usajili na michango, pamoja na kulinda maslahi ya wafanyakazi.
“Tunawahimiza waajiri kuitumia ipasavyo fursa hii kurekebisha hali zao za utii wa michango bila kuchelewa,” alisema. Aliongeza kuwa ATE imeendelea kusambaza taarifa za msamaha huo kwa wanachama wake kupitia mifumo yake ya mawasiliano, sambamba na kuendelea kutoa elimu na hamasa kwa waajiri ili kuhakikisha wanaitumia fursa hiyo kwa manufaa ya uendelevu wa biashara na ustawi wa sekta ya ajira kwa ujumla.




.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)
Na Nasra Ismail, Geita
MKURUGENZI Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita, Karia Rajab Magaro, Juni 25, 2026 ametembelea mradi wa ujenzi wa Soko la Kisasa Nkome Kata ya Nkome, Wilaya ya Geita. Lengo la ziara hiyo lilikuwa kujionea maendeleo ya mradi unaotarajiwa kuchochea biashara na ukuaji wa uchumi katika eneo hilo.
Akizungumza na mkandarasi wa mradi, kampuni ya RIN Contractor and General Supplies Company Ltd, Magaro amemuelekeza kuongeza kasi ya ujenzi ili mradi ukamilike na kukabidhiwa ifikapo mwishoni mwa Julai 2026 kama ilivyoelezwa kwenye mkataba.
Amesema Serikali inaendelea kusimamia kwa karibu utekelezaji wa miradi ya maendeleo ili wananchi wapate miundombinu bora inayokidhi mahitaji ya sasa na ya baadaye.
Mradi huo unafadhiliwa na Mgodi wa Dhahabu wa Geita - GGML kwa gharama ya Shilingi 473,909,792.82 hadi kukamilika. Ujenzi wa soko hilo unatarajiwa kuimarisha biashara, kuongeza ajira na kuinua kipato cha wananchi wa Nkome na maeneo jirani.
Akitoa taarifa ya maendeleo, Mhandisi wa mradi Eng. Edson Missana amesema soko hilo la kisasa litakuwa na uwezo wa kuhudumia wafanyabiashara na watumiaji zaidi ya 80 kwa wakati mmoja. Pia lina jengo la vyoo matundu 10 pamoja na mabafu maalumu kwa matumizi ya wafanyabiashara na wananchi.
Serikali imeeleza kuwa inaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuimarisha huduma za afya kwa wananchi wanaoathiriwa na mashambulizi ya wanyamapori katika Wilaya ya Serengeti, sambamba na kuchukua hatua za kudhibiti wanyama hatari wanaotoka kwenye hifadhi na kuingia katika makazi ya watu.
Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Dkt. Jafar Seif akijibu swali la Mbunge wa Serengeti, Mary Daniel Surati, ambaye alitaka kufahamu mkakati wa Serikali wa kuboresha huduma za afya kwa wananchi wanaokumbwa na madhara ya wanyamapori.
Dkt. seif amesema Serikali inatambua changamoto zinazowakabili wananchi wanaoishi au kufanya shughuli za kijamii katika maeneo yanayopakana na hifadhi zenye wanyamapori, ikiwemo Hifadhi ya Serengeti.
Amesema miongoni mwa mikakati inayotekelezwa ni kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu namna ya kujikinga dhidi ya wanyama hatari kama tembo, simba, chui na fisi, pamoja na kuhimiza utoaji wa taarifa kwa mamlaka husika mara wanapoonekana wakitoka hifadhini na kuingia kwenye makazi ya watu.
Aidha, Serikali imeendelea kuimarisha ufuatiliaji wa wanyamapori (surveillance) kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, wakiwemo Frankfurt Zoological Society (FZS) na Grumeti Reserves. Kupitia ushirikiano huo, wanyama wanaotoka nje ya hifadhi hufuatiliwa na kurejeshwa haraka ili kupunguza hatari kwa wananchi.
Katika kuimarisha huduma za afya, Waziri amesema Serikali inaendelea kujenga na kukarabati miundombinu ya kutolea huduma za afya, ikiwemo Hospitali ya Halmashauri ya Serengeti, vituo vya afya na zahanati. Hatua hiyo inalenga kuhakikisha wananchi wanaoishi karibu na maeneo ya hifadhi wanapata huduma bora za matibabu, ikiwemo kuwahudumia waathirika wa mashambulizi ya wanyamapori kwa wakati.
Serikali imesisitiza kuwa itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha usalama wa wananchi unaimarishwa huku huduma za afya zikiboreshwa ili kupunguza athari zinazotokana na migongano kati ya binadamu na wanyamapori.

Serikali itaendelea kushirikiana kwa karibu na wawekezaji wa sekta ya viwanda ili kutatua changamoto zinazokwamisha uzalishaji na kuweka mazingira bora yatakayochochea ukuaji wa uchumi wa viwanda nchini.
Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe.Judith Kapinga mara baada ya kufanya ziara katika kiwanda kikubwa cha kuchakata na kuzalisha mafuta ya kula cha Mainland Group Agro Process Tanzania jijini Dodoma, ambapo amejionea shughuli mbalimbali za uzalishaji na kiwango cha uwekezaji kilichofanyika katika kiwanda hicho.
Akizungumza baada ya kutembelea mitambo ya uzalishaji, Waziri Kapinga amesema Serikali inatambua mchango mkubwa wa sekta binafsi katika kukuza uchumi, kuongeza ajira na kuimarisha mapato ya Taifa, hivyo itaendelea kuhakikisha changamoto zinazowakabili wawekezaji zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati.
Amesema ameoneshwa kuvutiwa na uwekezaji mkubwa uliofanyika katika kiwanda hicho na kusisitiza kuwa viwanda vya kuongeza thamani ya mazao ya ndani vina nafasi muhimu katika kufanikisha malengo ya maendeleo ya Taifa pamoja na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
“Tunataka kuona mazao yanayozalishwa na wakulima wetu yanaongezewa thamani hapa hapa nchini. Hii ndiyo njia sahihi ya kuongeza tija kwa mkulima, mfanyabiashara, mwekezaji na Serikali kwa ujumla,” amesema Kapinga
Amebainisha kuwa licha ya Tanzania kuwa miongoni mwa wazalishaji wakubwa wa mazao ya mafuta, bado uzalishaji wa mafuta ya kula haujakidhi mahitaji ya ndani, hali inayolazimu nchi kuagiza sehemu ya mafuta kutoka nje.
Kutokana na hali hiyo, amesema Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali ikiwemo maboresho ya sera, sheria na mifumo ya kodi ili kuvutia uwekezaji zaidi katika viwanda vya mafuta ya kula na kuongeza uzalishaji wa ndani.
Waziri huyo amesema Serikali inalenga kuona nchi inafikia kujitosheleza kwa mafuta ya kula katika miaka ijayo kwa kuongeza uzalishaji wa malighafi na kuimarisha uwezo wa viwanda vilivyopo.
Katika mazungumzo yake na viongozi wa kiwanda hicho, ameelezwa kuwa changamoto kubwa inayokikabili ni upatikanaji mdogo wa malighafi, hususan mbegu za mazao ya mafuta, jambo linalofanya kiwanda kufanya kazi chini ya uwezo wake licha ya uwekezaji mkubwa uliowekwa.
Aidha, Serikali imeanza kushirikiana na Wizara ya Kilimo pamoja na taasisi zake kuweka mikakati ya kuongeza uzalishaji wa mazao ya mafuta ili kuhakikisha viwanda vinapata malighafi za kutosha na kutumia uwezo wake kikamilifu.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa kiwanda hicho, Bw. Jiaweli Chen, ameipongeza Serikali ya Tanzania kwa kuendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji na kutoa ushirikiano unaowezesha viwanda kufanya kazi kwa ufanisi na kuchangia maendeleo ya uchumi wa nchi.
Amesema kuwa sera na hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali zimeongeza imani kwa wawekezaji, jambo ambalo limechangia ukuaji wa shughuli za uzalishaji na kuongeza ajira kwa wananchi katika maeneo mbalimbali nchini.
Bw. Chen pia ameishukuru Serikali kwa kutembelea mradi huo na kusikiliza changamoto zinazowakabili, akieleza kuwa hatua hiyo inaonesha utayari wa viongozi kushirikiana na sekta binafsi katika kutafuta suluhisho la changamoto zinazojitokeza wakati wa utekelezaji wa shughuli za uzalishaji.
Hatahivyo amesema kuwa kiwanda hicho kitaendelea kushirikiana na Serikali katika kuongeza uzalishaji, kuimarisha ubora wa bidhaa na kuchangia jitihada za taifa za kukuza sekta ya viwanda, huku akieleza matumaini yake kuwa changamoto zilizowasilishwa zitapatiwa ufumbuzi kwa manufaa ya wawekezaji na wananchi kwa ujumla.









.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)








.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)



