Chuo cha Usafiri wa Anga (CATC) kwa niaba ya Shirika la Kimataifa la Usafiri wa Anga (ICAO) kimezindua rasmi mafunzo ya Vihatarishi katika Usafiri wa Anga (Risk Management Course) tarehe 20 Aprili 2026 jijini Dar es Salaam. Mafunzo haya ya siku tano yanawakutanisha washiriki 20 kutoka Tanzania, Uganda na Eswatini wakiwawakilisha mamlaka za viwanja vya ndege na mashirika ya ndege.

Lengo la mafunzo haya ni kuwajengea washiriki uwezo wa kutambua, kuchambua na kudhibiti vihatarishi vya kiusalama katika sekta ya usafiri wa anga, sambamba na kuimarisha utekelezaji wa viwango vya kimataifa vya usalama na kukuza ushirikiano wa kikanda.

Akizungumza wakati wa ufunguzi, Mkuu wa Chuo, Bw. Aristid Kanje, alisisitiza umuhimu wa mafunzo hayo katika kuimarisha usalama wa anga kikanda, akisema:

“ICAO imeweka viwango, sisi tunatekeleza. Mafunzo haya ya Vihatarishi katika Usafiri wa Anga (Risk Management Course) ni hatua muhimu katika kujenga ukanda wa anga unaotegemewa.”

Kwa upande wake, Mkufunzi wa CATC, Bi. Christine Bugoya, alielezea umuhimu wa mafunzo hayo kwa kina, akibainisha kuwa yatawaongezea washiriki mbinu za kitaalamu za usimamizi wa vihatarishi pamoja na kuboresha kwa mapana ushirikiano wa kiusalama baina ya nchi shiriki, hali itakayochangia kubadilishana uzoefu na kuimarisha mifumo ya usalama wa anga.

Kupitia mafunzo haya, Chuo cha Usafiri wa Anga (CATC) kinaendelea kuonesha dhamira yake ya kutoa mafunzo yenye viwango vya kimataifa na kuchangia kikamilifu katika kuimarisha usalama, ufanisi na maendeleo endelevu ya sekta ya usafiri wa anga kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Usafiri wa Anga (ICAO).
Mkuu wa Chuo cha Usafiri wa Anga (CATC), Aristid Kanje akifungua mafunzo ya Vihatarishi katika Usafiri wa Anga (Risk Management Course)  yaliyoanza tarehe 20 Aprili 2026 katika chuo hicho jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya Walimu pamoja na washiriki wa Mafunzo kutoka Tanzania, Uganda na Eswatini wakiwawakilisha mamlaka za viwanja vya ndege na mashirika ya ndege wakifuatilia hotuba ya mgeni rasmi wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya Vihatarishi katika Usafiri wa Anga (Risk Management Course)
Picha ya pamoja 


Na Vero Ignatus

BENY Israel Mwaisaka, mchungaji wa kanisa la FPCT Komwale lililopo nje kidogo ya mji wa Handeni, wilaya ya Handeni mkoani Tanga anasema kuwa ninatambua na kuthamini   Amani ambayo imekwepo tangu nchi ipate uhuru imekuwa msingi mkubwa wa maendeleo limewezesha wananchi kuishi kwa utulivu na kufanya shughuli zao bila hofu.

Kupitia amani hii, Watanzania wameweza kushiriki shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi kwa uhuru mkubwa. Michezo, biashara, elimu na ibada vimekuwa vikifanyika kwa utulivu mkubwa,vilevile Vijana wamepata nafasi ya kusoma na kujiendeleza, huku watu wa dini mbalimbali wakifanya ibada zao kwa uhuru. 

Haya yote ni matokeo ya juhudi za waasisi wa taifa letu ambao waliweka msingi wa umoja, mshikamano na upendo miongoni mwa Watanzania.

Mch.Mwaisaka anasema Amani ikikosekana hali hiyo huleta hofu kwa wananchi na kuhatarisha maendeleo katika sekta mbalimbali kama vile elimu, uchumi na hata uhuru wa kuabudu hivyo Ni muhimu kutambua kuwa amani si jambo la kudumu bila jitihada, bali inahitaji kulindwa na kila mmoja wetu kwa nguvu zote.

Katika mazungumzo mbalimbali ya kijamii, ndugu Hendry Lema, ambaye ni mzee mstaafu wa kanisa la KKKT Usharika wa Engarenaro Arusha, amekuwa akisisitiza umuhimu wa amani kwa maendeleo ya taifa. Anasema kuwa amani ndiyo nguzo kuu inayowezesha jamii kustawi, na bila amani hakuna maendeleo ya kweli yanayoweza kupatikana. 

"Mimi ni baba na Kichwa cha familia pia ni mlezi wa kiroho na mshauri wa jamii, nahimiza  watu kurejea katika misingi ya upendo, heshima na kuvumiliana, 

Ni wajibu wa kila Mtanzania kuhakikisha kuwa tunadumisha misingi hii ya upendo na mshikamano. Kama alivyotuasa hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, upendo ni silaha kubwa inayoweza kuondoa chuki, ubaguzi na migogoro.

 Tukizingatia hilo, tutaweza kujenga taifa lenye umoja na lenye kuheshimiana kati ya wananchi na viongozi wao, tutangulize utu ili kuepusha migongano isiyo ya lazima.

Mwisho, nitoe wito kwa Watanzania wote bila kujali dini au imani zao, kuendelea kuliombea taifa letu na kumtanguliza Mungu katika kila jambo. Tukiwa na moyo wa toba na unyenyekevu, 

Mungu atatusaidia kulinda amani yetu na kutujalia haki ya kweli. Kama ilivyoandikwa katika Mithali 14:34, “Haki huinua taifa; bali dhambi ni aibu ya watu wote.” Mungu ibariki Tanzania, Mungu tubariki Watanzania.

BENY Israel Mwaisaka, mchungaji wa kanisa la FPCT Komwale lililopo nje kidogo ya mji wa Handeni mkoani Tanga

 

Serikali imesisitiza umuhimu wa michezo kwa wafanyakazi kama sehemu muhimu ya kuimarisha afya na kuongeza ufanisi mahali pa kazi.

Wito huo umetolewa na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe.Rahma Kisuo, wakati akifungua rasmi Michezo ya Mei Mosi Kitaifa 2026 iliyofanyika Aprili 20, 2026 katika viwanja vya Sabasaba mkoani Njombe.

Amesema kuwa afya ya mfanyakazi ni mtaji mkubwa unaochangia maendeleo ya taasisi na taifa kwa ujumla, hivyo michezo inapaswa kupewa kipaumbele.

Aidha, Mhe.Kisuo amehimiza wafanyakazi kote nchini kujenga utamaduni wa kufanya mazoezi mara kwa mara badala ya kusubiri vipindi vya mashindano pekee. Amesisitiza kuwa mazoezi yawe sehemu ya maisha ya kila siku ili kuboresha afya na kuongeza tija kazini, huku akizitaka taasisi zote za umma na binafsi kuhakikisha zinatoa nafasi kwa wafanyakazi kushiriki shughuli za michezo.

Kwa upande wake Katibu Tawala wa mkoa wa Njombe Dkt. Stephane Nindi akimwakilisha Mkuu wa mkoa wa Njombe Mhe. Anthony Mtaka amesema kuwa, kufanyika kwa Maadhimisho ya Meimosi Njombe kumetoa fursa za kibiashara kwa wananchi wa mkoa huo.

Katika hatua nyingine, amewapongeza washiriki wa Michezo ya Mei Mosi na kuwataka kudumisha nidhamu, mshikamano na ushindani wa haki.

Amesisitiza kuwa michezo iwe chachu ya kuimarisha udugu na ushirikiano miongoni mwa wafanyakazi badala ya kuwa chanzo cha migogoro.

Kwa mwaka 2026, michezo hiyo inaongozwa na kauli mbiu isemayo, “Kazi zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050,” huku watumishi na wachezaji wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC) wakiwa miongoni mwa washiriki wa ufunguzi huo.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Mlezi wa Mtandao wa Wanawake Viongozi Afrika (AWLN) Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Liberia Mhe. Ellen Johnson Sirleaf mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 20 Aprili, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Mwanachama wa Mtandao wa Wanawake Viongozi Afrika (AWLN) Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Shirikisho la Kidemokrasia la Ethiopia Mhe. Sahle - Worke Zewde mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 20 Aprili, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Uongozi wa Mtandao wa Wanawake Viongozi Afrika (AWLN) uliongozwa na Mlezi wake Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Liberia Mhe. Ellen Johnson Sirleaf, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 20 Aprili, 2026.







Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza jambo na Mlezi wa Mtandao wa Wanawake Viongozi Afrika (AWLN) Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Liberia Mhe. Ellen Johnson Sirleaf pamoja na Mwanachama wa Mtandao huo, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Shirikisho la Kidemokrasia la Ethiopia Mhe. Sahle - Worke Zewde mara baada ya mazungumzo yao, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Aprili, 2026.






 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Uongozi wa Mtandao wa Wanawake Viongozi Afrika (AWLN), uliongozwa na Mlezi wake Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Liberia Mhe. Ellen Johnson Sirleaf pamoja na Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Shirikisho la Kidemokrasia la Ethiopia Mhe. Sahle - Worke Zewde, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Aprili, 2026.






Na Karama Kenyunko Michuzi Tv 

MWANAMKE  Monica Beda (36), mkazi wa Kimara jijini Dar es Salaam amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na shtaka la kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu kiasi cha shilingi milioni 60.

Katika hati ya mashtaka iliyosomwa mahakamani hapo leo Aprili 20,1026 na Wakili wa Serikali Cathbert Mbiling’i  imeileza mahakama kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo Novemba 8, 2025, katika Mtaa wa Samora, jijini Dar es Salaam.

Mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu Salome Mshasha, imedaiwa mshtakiwa alimlaghai Agrey Festo Mashanda kwa kujifanya angeweza kumuagizia gari aina ya Mitsubishi Fuso Fighter Damper lenye chassis namba  FK418F-550031, huku akijua kuwa si kweli.

Kwa mujibu wa upande wa mashtaka  upelelezi wa shauri hilo umekamilika na wameomba kupangiwa tarehe kwa ajili ya usikilizwaji wa awali (PH).

Hata hivyo mshtakiwa amekana kutenda kosa hilo na amerudishwa rumande kwa kushindwa kutimiza masharti ya dhamana 

Mahakama ilimpatia mshtakiwa dhamana kwa masharti ya kuwa na wadhamini wawili wa kuaminika, ambapo mmoja wao anatakiwa kuwasilisha hati ya mali isiyohamishika au fedha taslimu yenye thamani ya nusu ya fedha anazodaiwa kuiba, sawa na shilingi milioni 30.

Kesi hiyo limeahirishwa hadi Mei 6, 2026 kwa ajili ya mshtakiwa kusomewa maelezo ya awali.



Na Said Mwishehe,Michuzi TV

JUBILEE Health Insurance imetoa elimu kuhusu afya ya akili kwa wanafunzi wa Shule ya Sekondari Mzizima jijini Dar es Salaam lengo likiwa kuijengea uelewa jamii kuhusu afya ya akili huku ikieleza mpango huo utafanyika kwa wanafunzi wa shule mbalimbali nchini.

Akizungumza katika Shule ya Sekondari Mzizima jijini Dar es Salaam wakati wa kutolewa elimu kuhusu afya ya akili kwa wanafunzi 100 wa shule hiyo , Dk.Milembe Makoye ambaye ni Senior wellness officer kutoka Jubilee Health Insurance amesema wanaamini elimu ni ufunguo wa maisha hivyo wakielewa watajitambua.

“Tuko hapa kwa ajili ya kutoa elimu kuhusiana na afya ya akili lakini afya kwa ujumla.Kwanini tumeamua kutoa elimu hii ? Tunaamini wakielewa watajitambua.

“Kwanini afya ya akili ? Afya ya akili ni jambo ambalo ni changamoto kwa watu wengi sio kwa watu wazima pekee, lakini hata kwa watoto ambao wamekuwa wanasahaulika.

“Sasa kama Jubilee Health Insurance tunaamua kuingia kwenye jamii kuwagusa watoto wapate elimu sahihi waweze kujitambua ili hata wanapokua waweze kudhibiti changamoto ya matatizo ya afya ya akili lakini na afya ya mwili kwa ujumla,”amesema Dk.Makoye.

Aidha amesema Sekondari ya Mzizima ni ya kwanza kufikiwa lakini watakwenda shule nyingi zaidi kadri watakavyoweza huku akifafanua sababu za kuja na programu hiyo inatokana na ukweli Jubilee Health Insurance wanatoa huduma za bima ya afya.

“Lakini tukaona tusiishie kutoa tu bima basi tuguse jamii kwa kutoa elimu ya ustawi wa Afya, maana wakielewa maana ya afya ya akili watachukua njia sahihi ya kutunza afya zao na hapo tutakuwa tumefuzu.

Kwa upande wake Dkt.Isaac Marro akizungumza baada ya kutoa elimu ya afya ya akili kwa wanafunzi hao amesema kuna kila sababu ya Jamii kuwa na uelewa na afya ya akili mapema kwani kwa muda mrefu elimu kuhusu changamoto ya akili inatolewa kwa watu wazima.

“Kwa kifupi afya ya akili duniani kote imekuwa changamoto kubwa lakini tofauti na wenzetu ambao wao mapema waliwahi kubaini sisi tukachelewa.Kwahiyo changamoto zilipoanza kuwa kubwa na mapokeo yameendelea kuwa hasi.

Amesisitiza umuhimu kuzungumza kuhusu afya ya akili kuanzia umri mdogo wakiwemo watoto na vijana ili wajue, kwani hiyo inasaidia kutengeneza sio tu mbinu za kujilinda lakini pia kujilinda wenyewe kwa wenyewe.

Wakati huo huo Mshauri wa wanafunzi katika Sekondari ya Mzizima Theresia Mwaijala ametoa pongezi kwa Jubilee Health Insurance kwa kuona umuhimu wa kutoa elimu ya afya ya akili kwa wanafunzi.

“Juhudi zinazofanywa na Jubilee Health Insurance ni nzuri, wamekuja shuleni kwetu kuzungumza na wanafunzi kuhusu afya ya akili kitu ambacho ni muhimu kwasababu tunafahamu changamoto ya afya ya akili zinaanza mapema kuanzia miaka 14.

Hivyo amesema vizuri watoto wakapewa uelewa ,wafundishwe ili waweze kujilinda lakini wakiona kama kuna dalili ambazo zinaweza kusababisha afya ya akili wachukue hatua

Amesisitiza mafunzo ya Jubilee Health Insurance kuhusu afya ya akili kwa ujumla yanafaida kubwa ikiwemo kupata uelewa, na ukiwa na uelewa utachukua hatua sahihi.”



Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Waziri katika Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana, Joel Nanauka, amesema kuwa katika mwaka wa fedha 2026/2027, serikali itatekeleza mpango wake kwa kuzingatia vipaumbele vinne vikuu vinavyolenga kuimarisha maendeleo ya vijana nchini.

Akizungumza leo bungeni mjini Dodoma wakati akiwasilisha mpango na makadirio ya matumizi ya Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana, Nanauka alisema lengo kubwa la vipaumbele hivyo ni kuwawezesha vijana kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi, kijamii na kisiasa, pamoja na kuboresha ustawi wao kwa ujumla.

Kwa mujibu wa Nanauka, vipaumbele hivyo vitajikita katika maeneo yafuatayo:

Kwanza, kuimarisha ukuzaji wa biashara na uwezeshaji wa vijana kiuchumi, kwa lengo la kuwasaidia vijana wengi zaidi kujiajiri na kuajiriwa katika sekta za biashara na uzalishaji.

Pili, kuimarisha uratibu na ushirikishwaji wa vijana katika masuala ya kijamii, kiuchumi na kisiasa ili kuongeza ushiriki wao katika maendeleo ya taifa.

Tatu, kuimarisha uratibu wa elimu ya uraia, uzalendo pamoja na usimamizi wa shughuli za Mwenge wa Uhuru nchini.

Nne, kuimarisha ustawi na makuzi bora ya vijana ili kuhakikisha wanakua katika mazingira yanayowawezesha kufikia ndoto zao na kuchangia maendeleo ya taifa.

Nanauka alisisitiza kuwa mpango huo ni sehemu ya juhudi za serikali kuhakikisha vijana wanakuwa nguzo muhimu ya maendeleo ya taifa kupitia fursa za kiuchumi na ushiriki mpana katika ujenzi wa nchi.



Na Janeth Raphael

Serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo imesema kuwa mpango wa mkopo wa shilingi bilioni 20 uliotengwa kwa ajili ya kuwawezesha watengenezaji wa maudhui mitandaoni (content creators) umeonyesha mwitikio mkubwa kuliko ilivyotarajiwa, hali inayoashiria ongezeko kubwa la vijana wanaojihusisha na sekta ya ubunifu wa kidigitali nchini.

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya utiaji saini wa makubaliano ya Tanzania kuwa mwenyeji wa Mashindano ya 74 ya Miss World 2027, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, amesema lengo la mkopo huo ni kuwawezesha vijana wenye vipaji lakini wenye changamoto za kifedha ili waweze kukuza ubunifu wao na kujiajiri kupitia maudhui ya kidigitali.

Makonda amesema mpango huo ulipangwa kwa nia ya kuwasaidia vijana wanaoanza safari yao ya ubunifu, hasa wale wanaokosa vifaa muhimu kama kamera bora, vifaa vya uhariri, na rasilimali nyingine za msingi zinazohitajika katika uzalishaji wa maudhui ya kisasa.

Hata hivyo, amesema tathmini ya awali imeonesha kuwa maombi yamezidi kiwango kilichotarajiwa, jambo linaloonesha wazi kuwa sekta ya content creation imekuwa na mvuto mkubwa na inakua kwa kasi nchini Tanzania.

“Hatuwezi kuchukua mkopo huu tukawapa watu ambao tayari wana uwezo mkubwa, kama kumiliki magari ya gharama kubwa au kuwa na vifaa vya kisasa. Dhamira yetu ni kumsaidia kijana wa kawaida aliye mtaani, mwenye ndoto lakini hana uwezo wa kuanza,” amesema Makonda.

Kutokana na hali hiyo, Waziri huyo amesema serikali imeamua kuahirisha kwa muda utekelezaji wa mpango huo ili kufanya maboresho muhimu, yakiwemo marekebisho ya vigezo na masharti ya mkopo huo ili kuhakikisha unawafikia walengwa sahihi.

Ameongeza kuwa maboresho hayo yatalenga pia kuweka riba nafuu na masharti rahisi zaidi ili kuhakikisha mkopo huo hauwi mzigo kwa vijana, bali unakuwa kichocheo cha ukuaji wa sekta ya ubunifu na ajira nchini.

Serikali imesisitiza kuwa dhamira yake ni kuhakikisha vijana wengi zaidi wananufaika na fursa zilizopo kwenye uchumi wa kidigitali, ambao kwa sasa unaendelea kukua kwa kasi na kutoa nafasi kubwa za ajira na ubunifu.



Top News