Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Umoja wa Afrika na Mkuu wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa katika Umoja wa Afrika (UNOAU), Bw. Parfait Onanga-Anyanga amewasili nchini kwa ziara akiwa kama Mjumbe Maalum wa Mhe. Antonio Guterres, Katibu Mkuu UN kwenye ziara ya kikazi lengo likiwa ni kukutana na kufanya mazungumzo na Mamlaka pamoja na wadau mbalimbali kuhusu matukio yaliyotokea kabla na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Tanzania, 2025 na kuangalia hali ya maisha ya Tanzania kwa sasa.

Bw. Onanga-Anyanga ametoa pongezi hizo alipofanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.), jijini Dar es Salaam, ikiwa ni hatua ya mwanzo ya mazungumzo yake na Serikali pamoja na wadau mbalimbali wa kitaifa.

Mjumbe huyo yupo nchini kwa ziara ya kikazi kwa lengo la kufanya mashauriano na Serikali na wadau wengine wa kitaifa kuhusu hali ya kisiasa nchini, pamoja na kujadili namna Umoja wa Mataifa unavyoweza kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuimarisha taasisi za kidemokrasia, kusimamia mageuzi na kuendeleza umoja na mshikamano wa kitaifa kupitia maridhiano jumuishi.

Aidha, amempongeza Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuonesha utulivu na uongozi makini katika kipindi hicho kigumu kwa taifa. Amekaribisha pia uamuzi wa Serikali wa kuunda Tume ya Kuchunguza Matukio Wakati na Baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025

Bw. Onanga-Anyanga aliipongeza Tume hiyo inayoongozwa na Mhe. Mohamed Chande Othman, Jaji Mkuu Mstaafu kwa kazi yake nzuri yenye kubeba uzito na ubobezi na viwango vya hali ya juu na ya kuigwa kimataifa. Ameeleza pia kuwa muundo wa Tume hiyo unaojumuisha wajumbe kutoka kada mbalimbali umeongeza ubora na uhuru wa kazi yake.

Aidha, ameipongeza Serikali kwa juhudi zake za kurejesha imani ya wananchi na kudumisha utulivu baada ya matukio hayo, pamoja na hekima na utulivu uliotumika katika kushughulikia changamoto zilizojitokeza wakati wa kipindi cha uchaguzi.

Katika muktadha huo, Mwakilishi huyo Maalum alikaribisha mpango mpana wa kitaifa uliotangazwa na mamlaka mwezi Januari 2026 chini ya kaulimbiu ya “Repair – Rebuild – Renew,” akibainisha kuwa mpango huo unaweka msingi muhimu wa kuimarisha utawala wa kidemokrasia, kusimamia mageuzi ya taasisi pamoja na kuendeleza maridhiano ya kitaifa.

Vilevile, amempongeza Mhe. Mahmoud Kombo, kwa juhudi zake za kuielezea jumuiya ya kimataifa hatua na michakato ya ndani ya nchi inayochukuliwa kushughulikia matukio hayo na kuimarisha mshikamano wa kitaifa.

Katika ratiba ya ziara yake nchini, Bw. Onanga-Anyanga anatarajiwa kukutana na viongozi wa vyama vya siasa ikiwemo Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), ACT Wazalendo, Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMA) na Chama Cha Mapinduzi (CCM) ili kubadilishana mawazo kuhusu masuala ya utawala bora, demokrasia na mshikamano wa kitaifa.

Aidha, atafanya mazungumzo na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jaji Mkuu pamoja na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambani ni wawakilishi wa mihimili yote mitatu ya dola.

Kwa upande wake, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.) ameishukuru Umoja wa Mataifa kwa ushirikiano wake na kueleza kuwa Tanzania inathamini sana ushirikiano huo. Ameeleza kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na UN na haitasita kuomba msaada wake pale inapohitajika katika kuimarisha taasisi za taifa na kulinda amani, utulivu na mshikamano wa wananchi.













Na Munir Shemweta, Masasi

Mbunge wa Jimbo la Masasi na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo, amekabidhi vifaa tiba katika Kituo cha Afya Mbonde kilichopo Halmashauri ya Mji Masasi mkoani Mtwara kwa lengo la kuimarisha utoaji wa huduma za afya kwa wananchi.

Dkt. Akwilapo amekabidhi vifaa hivyo leo, Machi 9, 2026, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha huduma za afya katika Wilaya ya Masasi na maeneo jirani ya wilaya hiyo.

Akizungumza wakati wa kukabidhi vifaa hivyo, Dkt. Akwilapo amesema utoaji wa vifaa tiba ni sehemu ya jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita kuhakikisha taasisi za huduma za jamii kama vile hospitali na shule zinakuwa na miundombinu na vifaa vinavyowawezesha wataalamu kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Amesema, serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha sekta za afya na elimu zinaimarika ili wananchi waweze kupata huduma bora karibu na maeneo yao.

“Naishukuru serikali chini ya Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuhakikisha siyo tu inajenga majengo ya hospitali na shule, bali pia inahakikisha kunapatikana vifaa pamoja na wataalamu watakaowezesha huduma kutolewa kwa ufanisi,” amesema Dkt. Akwilapo.

Ameongeza kuwa, kupatikana kwa vifaa tiba katika Kituo cha Afya Mbonde, ikiwemo mashine maalum ya kusaidia watoto waliozaliwa kabla ya muda, kutasaidia kuokoa maisha ya watoto hao.

Kwa upande wake, Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Mbonde, Dkt. Mohamed Abbas, amesema, vifaa vilivyopokelewa vitasaidia kuimarisha huduma mbalimbali ikiwemo huduma kwa watoto, chumba cha upasuaji pamoja na huduma za maabara.

Kwa mujibu wa Dkt Abbas, kituo hicho cha afya Mbonde kinahudumia zaidi ya wananchi 32,000 kutoka kata tatu za Sululu, Mtawale na Mwenge Mtapika. Pia kituo kinatoa huduma kwa wagonjwa wanaotoka Halmashauri za Masasi na Nanyumbu.

Dkt. Abbas ameongeza kuwa, kituo hicho kinatoa huduma mbalimbali zikiwemo upasuaji, huduma za kulaza wagonjwa, uzazi pamoja na maabara.

Katika hatua nyingine, Mbunge huyo wa Jimbo la Masasi na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Leonard Akwilapo pia amekabidhi vitabu 3,667 kwa shule 12 za Halmashauri ya Mji Masasi kwa lengo la kusaidia shughuli za ufundishaji na ujifunzaji.

Akizungumza wakati wa kukabidhi vitabu hivyo Machi 9, 2026, mara baada ya kukutana na watendaji wa sekta ya elimu katika halmashauri hiyo, Dkt. Akwilapo amesema vitabu ni nyenzo muhimu katika kuboresha elimu shuleni.

“Kama tunavyojua, ufundishaji unahitaji zana, na moja ya zana muhimu ni vitabu. Hii ni awamu ya kwanza ya msaada huu na tutakuja tena na awamu ya pili, lengo ni kuwapa walimu nafasi ya kufanya kazi kwa ufanisi zaidi,” amesema.

Amesema, hatua hiyo inalenga kuimarisha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji ili kuongeza ubora wa elimu kwa wanafunzi wa shule hizo.

Mbunge wa Jimbo la Masasi na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akimkabidhi moja ya vifaa tiba Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Mbonde kilichopo Masasi mkoani Mtwara Dkt Mohamed Abbas wakati wa ziara yake mkoani humo.
Mbunge wa Jimbo la Masasi na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akipata maelezo ya moja ya kifaa tiba kutoka kwa Mganga Mfawadhi wa Kituo cha Afya Mbonde Dkt Mohamed Abbas wakati wa ziara ya Jimbo tarehe 9 Machi 2026.
Mbunge wa Jimbo la Masasi na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo pamoja na viongozi wengine wakiwa katika picha na moja ya vifaa tiba alivyokabidhi katika hospitali ya Mbonde Masasi tarehe 9 Machi 2026.
Mbunge wa Jimbo la Masasi na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akisalimiana na mmoja wa wagonjwa waliokwenda kupata huduma katika Kituo cha Afya Mbonde Masasi mkoani Mtwara tarehe 9 Machi 2026. Mbunge wa Jimbo la Masasi na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akimkabidhi vitabu mmoja wa walimu wa shule za sekondari katika halmashauri ya Mji Masasi alipotoa vitabu 3,667 kwa sekondari za halmashauri hiyo tarehe 9 Machi 2026.
Mbunge wa Jimbo la Masasi na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akionesha moja ya vitabu alivyokabidhi kwa shule za sekondari mara baada ya kuvikabidhi tarehe 9 Machi 2026.Mbunge wa Jimbo la Masasi na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akiwa katika picha ya pamoja na watendaji wa sekta ya elimu katika halmashauri ya Mji Masasi mara baada ya kukabidhi vitabu 3,667 kwa shule za sekondari tarehe 9 Machi 2026.
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Geita, imewapandisha kizimbani Wabunge wa Jimbo la Chato Kaskazini na Chato Kusini, pamoja na Madiwani wanne wa Halmashauri ya Wilaya ya Chato kwa tuhuma za vitendo vya rushwa.

Akizungumza leo Machi 9, 2026, Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Geita, James Ruge, amebainisha kuwa viongozi hao wamefikishwa mahakamani kufuatia uchunguzi uliothibitisha kuwepo kwa mchezo mchafu wa ushawishi.

Inadaiwa kuwa viongozi hao waliwakusanya madiwani wateule 20 wa Chato katika hoteli ya Lake Zone jijini Mwanza, na baadaye katika hoteli ya Serengeti Palace iliyopo Katoro, Geita. Lengo la mkusanyiko huo lilikuwa ni kuwashawishi madiwani hao kwa, Hongo ya fedha,Chakula na Malazi, Kupiga kura za upendeleo kwa mgombea waliyemtaka katika nafasi ya Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Chato.

Mbinu za Kumng'oa Mpinzani

Katika tuhuma nyingine, Mbunge wa Chato Kusini akishirikiana na aliyekuwa Diwani mteule wa Bwongera, Bartholomeo Christian Manunga, na Josephat Elias Manyenye (Kata ya Bwera), wanatuhumiwa kujenga ushawishi wa rushwa.

Walimlenga aliyekuwa Diwani mteule wa Kata ya Muungano, Njile Charles Mboligo, kwa kumpa hongo ili ajiondoe kwenye kinyang'anyiro cha uenyekiti. Lengo lilikuwa kumpatia ushindi wa wazi Bartholomeo Manunga katika mchakato huo ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).

TAKUKURU imeeleza kuwa hatua hizo za kisheria zimechukuliwa chini ya Sheria ya Kupambana na Rushwa Sura ya 329 (Marejeo ya 2023) kama ilivyorekebishwa na Sheria Na. 11 ya mwaka 2024.

Uchunguzi ulibaini kuwa mchakato huo wa uchaguzi ndani ya chama ulitawaliwa na harufu ya rushwa, jambo lililopelekea watuhumiwa wote kufikishwa mahakamani leo Machi 9, 2026.








📍Amtuma MwanaFA na shilingi milioni 10


Na Mashaka Mhando

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amemtumia salamu za faraja na mkono wa heri nguli wa muziki wa dansi nchini, Mzee Zahir Ally Zorro, ambaye kwa sasa anakabiliwa na changamoto za kiafya.

Salamu hizo za Rais zimefikishwa nyumbani kwa mwanamuziki huyo Kisota, Kigamboni Jijini Dar es salaam leo na Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma (MwanaFA). Katika ziara hiyo, Mhe. Mwinjuma alipokelewa na Mzee Zahir Zorro pamoja na mwanawe, mwanamuziki nyota wa R&B, Banana Zorro.

Akizungumza kwa niaba ya Rais, Mhe. Mwinjuma alisema kuwa Mkuu wa Nchi ameguswa na hali ya Mzee Zorro na ametambua mchango wake usiofutika katika utamaduni na sanaa ya Tanzania.

"Nimetumwa na Mheshimiwa Rais kuja kukujulia hali na kukushika mkono. Rais anajua mchango wako na ameelekeza nikukabidhi kiasi hiki cha Shilingi Milioni 10 kusaidia taratibu zako za matibabu na mahitaji mengine," alisema Mhe. Mwinjuma.

Kwa upande wake, mwanamuziki Banana Zorro, aliishukuru serikali kwa niaba ya familia kwa kumkumbuka baba yao katika kipindi hiki ambacho pia familia bado inakabiliwa na majonzi ya kuondokewa na binti yao, Maunda Zorro miaka kadhaa iliyopita.

Mzee Zahir Zorro, ambaye ni mmoja wa magwiji wa mwisho wa kizazi cha dhahabu cha muziki wa Dansi nchini, alitoa shukrani za dhati kwa Rais Samia, akibainisha kuwa upendo huo unampa nguvu na matumaini ya kurejea katika hali yake ya kawaida.

Ziara hiyo imetafsiriwa na wadau wa sanaa kama ishara ya utu na utambuzi wa dhati wa mchango wa wasanii wakongwe walioasisi sanaa ya kisasa nchini.







Na Farida Mangube, Morogoro


Wanawake wametakiwa kutumia kikamilifu fursa za masomo na mafunzo zinazotolewa na Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) ili kujijengea uwezo, kuongeza ujuzi, na kuimarisha ushiriki wao katika maendeleo ya jamii.

Wito huo umetolewa na Naibu Makamu Mkuu wa Chuo upande wa Mipango, Fedha na Utawala, Prof. Amandus Muhairwa, wakati wa hafla ya kuwapongeza wanawake wa chuo hicho katika maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani.

Prof. Muhairwa amesema kuwa chuo kina mfumo thabiti wa kulinda wanawake na wasichana pamoja na kutekeleza mpango mkakati wa usawa wa kijinsia, hali inayochangia kuwepo kwa mazingira salama, yenye utulivu na yanayowezesha wanawake kufikia malengo yao ya kitaaluma na kiutendaji.

Kwa upande wao, Mwenyekiti wa RAAWU tawi la SUA, Bw. Faraja Kamendu, na Mwenyekiti wa THTU tawi la SUA, Bw. Nickson Mkilamwene, wamesema kuwa kuwapa wanawake nafasi katika ajira na uongozi kunachochea ufanisi wa utendaji kazi katika taasisi mbalimbali.

Viongozi hao pia wamewahamasisha wanawake kufanya kazi kwa bidii kwa maendeleo ya chuo na kujiunga na vyama vya wafanyakazi ili kulinda maslahi yao ya kikazi na kitaaluma.

Akisoma hotuba kwa mgeni rasmi kwa niaba ya wanawake wa chuo hicho, Bi. Farida Mkongwe ameishukuru menejimenti ya chuo kwa kuendelea kutoa fursa za mafunzo kwa wanawake, akisema hatua hiyo imechangia kwa kiasi kikubwa kuongeza ujuzi, uwezo na weledi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kazi.

Ameongeza kuwa utoaji wa mafunzo kwa watumishi unazingatia mipango na bajeti ya chuo, huku akiiomba menejimenti kuendelea kupanua wigo wa fursa hizo ili kuwajengea wanawake uwezo zaidi katika nyanja mbalimbali za kitaaluma na kiutendaji.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mhe. Adam Malima, amesema mkoa huo umeendelea kuwa kinara katika kuwawezesha wanawake kiuchumi kama sehemu ya kutambua mchango wao muhimu katika maendeleo ya jamii.

Akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyofanyika kimkoa katika viwanja vya Shule ya Msingi Fulwe, Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro, Malima amekemea tabia ya baadhi ya watendaji wa serikali kuvumilia vitendo vya unyanyasaji dhidi ya wanawake, hususan wanapopoteza wenza wao.

Amesisitiza umuhimu wa kuchukua hatua kali za kisheria dhidi ya vitendo hivyo ili kulinda haki, usalama na ustawi wa wanawake katika jamii.








WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema kuwa Serikali inatambua uwepo wa watumishi wa umma wanaochapakazi na kuwataka kuendelea kufanya kazi kwa bidii na uadilifu huku wakijiepusha kujiingiza katika makundi ya wazembe, wezi na wanaofanya kazi kwa mazoea.

“Serikali haitomuonea mtu, watumishi wachapakazi wasiingie ubaridi kwa sababu Serikali inatambua mchango wao katika maendeleo ya Taifa. Watu wasome alama za nyakati Serikali haitovumilia masuala ya wizi kwa sababu yanarudisha nyuma maendeleo.”

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo Jumatatu, Machi 09, 2026 wakati akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika kata ya Namanyere wilayani Nkasi akiwa katika ziara ya kikazi mkoani Rukwa. Miongoni mwa malengo ya ziara hiyo ni kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Dkt. Mwigulu ametumia fursa hiyo kuwasisitiza watumishi wa umma kufanya kazi kwa weledi na kujiepusha na vitendo vya udokozi kwa sababu havikubaliki na havivumiliki, hivyo wahakikishe wanatekeleza majukumu yao ikiwemo kusimamia ipasavyo ujenzi wa miradi.

Pia, Waziri Mkuu amesisitiza mikoa yote kuhakikisha katika upangaji wa bajeti wanaweka vipaumbele vya uchimbaji wa visima kupitia mitambo iliyosambazwa katika mikoa yao. “Mitambo ya uchimbaji maji itumike kuchimba visima ili wananchi wapate maji ya uhakika.”

Wakati huo huo, Waziri Mkuu amezitaka mamlaka husika kuangalia uwezekano wa kuweka utaratibu au sheria itakayowabana wakandarasi kuhakikisha wanawalipa wafanyakazi wao stahiki zao kwa wakati.

Ametoa agizo hilo kutokana na kumekuwapo kwa malalamiko ya baadhi ya wakandarasi kutowalipa wafanyakazi wanaofanya kazi katika miradi ya ujenzi hata pale wanapokuwa wameshalipwa na Serikali kwa kazi walizotekeleza.

Mheshimiwa Dkt. Mwigulu ametoa agizo hilo baada ya wananchi waliofanykazi katika miradi mbalimbali kueleza kero ya kutolipwa na wakandarasi licha ya wakandarasi hao kuwa tayari wamelipwa na Serikali.

Kwa upande wao, wabunge wa mkoa wa Rukwa wameipongeza Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa utekelezwaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika maeneo yao ikiwemo ya afya, elimu na kilimo.

Miongoni mwa wabunge hao ni Mbunge wa Nkasi Kaskazini Salum Kazukamwe ambaye alishukuru kwa ujenzi wa hospital ya wilaya ambayo inakwenda kurahisisha upatikanaji wa huduma bora za afya, ambapo pia, mbunge huyonameiomba Serikali kumalizia ujenzi wa kituo cha afya cha Kebwe.





Wanawake wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) wameungana na wanawake wengine kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani 2026, katika maadhimisho ya kimkoa yaliyofanyika Machi 8, 2026 katika Viwanja vya Barafu Mburahati, Wilaya ya Ubungo jijini Dar es Salaam.

Maadhimisho hayo yalihudhuriwa na wanawake kutoka taasisi mbalimbali za umma na binafsi, ambapo Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila, alikuwa mgeni rasmi katika hafla hiyo.

Akizungumza wakati wa maadhimisho hayo, Mhe. Chalamila aliwahimiza wanawake kuendelea kutumia fursa zilizopo ili kujiendeleza kiuchumi na kuchangia kikamilifu katika maendeleo ya taifa.

Alisema wanawake wana nafasi kubwa katika maendeleo ya jamii na taifa, hivyo ni muhimu waendelee kupewa na kutumia kikamilifu fursa zilizopo kwa ajili ya kufikia maendeleo jumuishi.

“Wanawake wana mchango mkubwa katika maendeleo ya jamii na taifa, hivyo ni muhimu waendelee kupewa na kutumia kikamilifu fursa zilizopo ili kufikia maendeleo jumuishi,” alisema Chalamila.

Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Wanawake TUICO tawi la NBAA Bi. Irene Mutagaywa amesema kuwa kaulimbiu ya maadhimisho hayo ambayo ni “Haki na usawa kwa wanawake na wasichana,” inalenga kuhamasisha jamii kuhakikisha wanawake na wasichana wanapata haki na fursa sawa katika nyanja mbalimbali za maisha, jambo ambalo pia linaendana na malengo ya maendeleo ya kimataifa kuelekea mwaka 2030 na ajenda ya maendeleo ya mwaka 2050.

Pia amesema maadhimisho hayo yamekuwa jukwaa muhimu la kuwakutanisha wanawake kutoka sekta mbalimbali kujadili masuala ya usawa wa kijinsia, haki za wanawake pamoja na mchango wao katika maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.

Siku ya Wanawake Duniani huadhimishwa kila mwaka tarehe 8 Machi, ikiwa ni siku maalum ya kutambua mchango wa wanawake katika jamii na kuendelea kuhamasisha usawa wa kijinsia.

Historia ya siku hiyo inaanzia mwaka 1908, ambapo wanawake takribani 15,000 waliandamana katika mji wa New York, Marekani, wakidai kupunguziwa muda wa kazi, ujira wa kuridhisha na haki ya kupiga kura. Mwaka uliofuata, chama cha kisoshalisti cha Amerika kilitangaza siku ya kwanza ya kitaifa ya wanawake.

Wazo la kuifanya kuwa Siku ya Wanawake Kimataifa lilianzishwa mwaka 1910 na mwanaharakati wa haki za wanawake Clara Zetkin, wakati wa mkutano wa kimataifa wa wafanyakazi wanawake uliofanyika Copenhagen, Denmark.






Picha mbalimbali za matukio ya wafanyakazi wanawake wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) katika maadhimisho ya Siku ya wanawake Kimataifa yaliyofanyika Machi 08, 2025 katikaViwanja vya Barafu Mburahati, Wilaya ya Ubungo jijini Dar es Salaam.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe. Albert Chalamila pamoja na viongozi mbalimbali wakiwapungia mikono wafanyakazi wanawake wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) katika maadhimisho ya Siku ya wanawake Kimataifa.


Top News