Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM) leo imepokea ujumbe wa wadau wa maendeleo kutoka taasisi mbalimbali ikiwemo Mastercard Foundation, Education for Sub-Saharan Africa (ESSA), Tanzania Education Network (TEN/MET), African Centre for School Leadership (ACSL), Teach United na Educate kwa ajili ya kujadili ushirikiano wa kuimarisha uongozi wa shule za sekondari nchini.

Akifungua kikao hicho, Mtendaji Mkuu wa ADEM, Dkt. Maulid J. Maulid, alieleza kuwa taasisi hiyo ina dhamana ya kitaifa ya kuwa kitovu cha ubora katika mafunzo, utafiti na ushauri kuhusu uongozi, usimamizi, utawala wa elimu pamoja na uhakiki wa ubora wa elimu.

Alisema kwa miongo kadhaa ADEM imekuwa mkono wa kimkakati wa Serikali katika kujenga uwezo wa wasimamizi wa elimu kuanzia wakuu wa shule, waratibu wa elimu wa kata, hadi maafisa wa elimu wa wilaya, mikoa na ngazi ya taifa.

“ADEM haijikiti tu kwenye mafunzo bali pia inafanya tafiti za kitaaluma zinazosaidia kuunda sera za elimu, kutoa huduma za ushauri kwa shule na halmashauri pamoja na kuandaa mifumo na zana za kuboresha utendaji wa shule. Kupitia mtandao mpana wa taasisi na maafisa wa elimu katika Mamlaka zote za Serikali za Mitaa, ADEM ina uwezo wa kutekeleza programu kubwa za kuimarisha uongozi na usimamizi wa shule nchini,” alisema Dkt. Maulid.

Katika kikao hicho, ADEM iliwasilisha maeneo yake muhimu ya utaalamu ikiwemo uongozi na utawala wa elimu, upangaji wa sera na uhakiki wa ubora, mipango ya maboresho ya shule, ufundishaji unaozingatia usawa wa kijinsia, uongozi wa kitaaluma wa ufundishaji, maendeleo ya taaluma ya walimu, ushirikishwaji wa jamii katika usimamizi wa shule pamoja na ufuatiliaji na tathmini ya mipango ya kimkakati ya shule.

Majadiliano pia yalijikita katika utekelezaji wa programu ya LIT-LEAD, inayotekelezwa kwa ushirikiano kati ya ADEM na VVOB – Education for Development kwa ufadhili wa Mastercard Foundation.

Programu hiyo inalenga kuziba pengo la uongozi katika shule za sekondari nchini kwa kuwajengea uwezo wakuu wa shule katika kuboresha ufundishaji na ujifunzaji, kukuza uongozi jumuishi unaozingatia usawa wa kijinsia, kuimarisha mipango ya maboresho ya shule pamoja na kuboresha utawala wa shule kupitia ushiriki wa kamati za shule na wazazi.

Kabla ya kuanza kwa utekelezaji wa programu hiyo, ADEM na VVOB zilifanya tathmini ya mahitaji ya mafunzo (Training Needs Assessment - TNA) iliyowahusisha viongozi wa shule, maafisa wa elimu wa wilaya pamoja na wawakilishi wa Wizara ili kuhakikisha maudhui ya mafunzo yanaendana na mazingira halisi ya elimu nchini Tanzania.

Akizungumza katika kikao hicho, Mkurugenzi wa VVOB nchini Tanzania, Bi. Sarish Hiribae, alipongeza ushirikiano uliopo kati ya VVOB na ADEM katika kuimarisha uongozi wa shule za sekondari nchini.

Kwa upande wake, kiongozi wa ujumbe wa wadau kutoka Mastercard Foundation, Bi. Tracy Osio, aliipongeza ADEM kwa ushirikiano wake na VVOB pamoja na wadau wengine, akieleza kuwa ushirikiano huo una uwezo mkubwa wa kuleta mageuzi katika uongozi wa elimu kupitia utekelezaji wa programu ya LIT-LEAD.

Katika majadiliano hayo, wadau pia waliuliza maswali kuhusu mifumo ya ADEM ya kuhakikisha ubora wa mafunzo yanayotolewa. Kujibu hilo, ADEM ilieleza kuwa ubora wa mafunzo huhakikishwa kupitia tathmini za mahitaji ya mafunzo, warsha za uthibitishaji wa maudhui pamoja na uhakiki wa ubora unaofanywa na Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET) kwa kozi za muda mrefu.

Aidha, Dkt. Lucas Mzelela alieleza kuwa ushirikiano kati ya ADEM na VVOB ulianza mwaka 2025 na unatarajiwa kudumu kwa kipindi cha miaka sita. Katika kipindi hicho, taasisi hizo zitashirikiana kujenga uwezo wa wakuu wa shule za sekondari katika uongozi bora na usimamizi madhubuti wa elimu.

Aliongeza kuwa ushirikiano huo pia utahusisha uandaaji wa moduli za mafunzo kupitia mfumo wa kidijitali wa Learning Management System (LMS) ili kuwafikia viongozi wengi zaidi wa elimu nchini.

Kupitia ushirikiano wa kimkakati kama programu ya LIT-LEAD, ADEM inaendelea kuwa mhimili muhimu katika kuendeleza ajenda ya taifa ya kuboresha elimu na kuimarisha uongozi wa shule kwa manufaa ya wanafunzi nchini.










Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu - ADEM umeendesha mafunzo maalumu ya siku tano kwa Maafisa Elimu wa Mikoa 26 kutoka Tanzania Bara kuanzia tarehe 8-12 Machi, 2026 jijini Arusha.

Mafunzo hayo yalilenga kuwajengea uwezo viongozi hao wa kuimarisha uongozi na usimamizi wa sekta ya elimu katika maeneo mbalimbali ikiwemo uandaaji wa Mpango Mkakati wa elimu katika ngazi ya mkoa, utafutaji na usimamizi wa rasilimali katika elimu, utambuzi na usimamizi wa changamoto za afya ya akili kwa watumishi wa kada ya elimu, mbinu bora za kushughulikia malalamiko, kufanya ufunzaji na uatamizi, na kuimarisha usimamizi saidizi katika sekta ya elimu.

Akifunga mafunzo hayo, Kamishna wa Elimu nchini, Dkt. Lyabwene M. Mtahabwa, amesisitiza umuhimu kwa viongozi wote wa elimu kuanzia ngazi ya kitaifa hadi shule kuweka mbele haki za watoto katika utekelezaji wa majukumu yao.

Amesema kuwa watoto ndio msingi wa uwepo wa nafasi za uongozi katika sekta ya elimu, hivyo viongozi wanapaswa kuhakikisha wanawalinda na kuwapatia mazingira bora ya kujifunzia.

Aidha, Dkt. Mtahabwa amewataka Maafisa Elimu wa Mikoa kuacha mtindo wa uongozi unaolenga kutafuta makosa kwa nia ya kuwaadhibu wanaowaongoza na badala yake, amewahimiza kutumia mbinu za kutoa msaada wa kitaaluma na kitaalamu kwa watumishi wa elimu, kama walivyojifunza wakati wa mafunzo hayo.

“Ni muhimu viongozi wa elimu kuwa washauri na wawezeshaji kwa wale wanaowaongoza, badala ya kuwa wakaguzi wanaotafuta makosa,” Amesisitiza Dkt. Mutahabwa

Kamishna wa elimu pia, amesisitiza kuwa Serikali pamoja na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kupitia taasisi zake ikiwemo ADEM, imejipanga kuhakikisha mtoto wa Kitanzania anapata elimu bora katika mazingira salama.

Amesema ili kufikia lengo hilo, kila kiongozi wa elimu anapaswa kusimamia kikamilifu majukumu yake katika eneo analoliongoza.

Mafunzo hayo ni sehemu ya jitihada za Serikali kuendelea kuimarisha uwezo wa viongozi wa elimu ili kuboresha utoaji wa elimu nchini.

Jumla ya Maafisa Elimu wa Mikoa 26 kutoka katika Mikoa yote ya Tanzania Bara wameshiriki mafunzo hayo yaliyoendeshwa na ADEM kwa ufadhili wa mradi wa Shule Bora.












Na Mwandishi wetu, Tabora

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imeridhishwa na Ujenzi wa Kiwanda cha Zege kinachomilikiwa na kampuni tanzu ya TANESCO ya  kuzalisha nguzo za zege  kilichopo katika Mkoa wa Tabora wakati wa ziara yao ya kikazi Mkoani humo tarehe 12 Machi, 2026.

Akizungumza baada ya ziara hiyo Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Subira Mgallu ameeleza kuridhishwa na   hatua ya kukamilika kwa Kiwanda hicho kilichoanza uzalishaji  na kuwaelekeza Wizara ya Nishati  na TANESCO kukisimamia kiwanda hiko kiendelee kufanya kazi kwa ufanisi mkubwa na kuzalisha faida.

"Kwa niaba ya Kamati tumeridhika na kazi kubwa iliyofanyika katika kiwanda hiki ambacho kimekamilika na uzalishaji umeanza, tunatoa rai kwa Wizara na TANESCO kuendelea kusimamia kiwanda hiki ili kiendelee kufanya kazi yake kwa ufanisi zaidi", alieleza Mhe. Mgallu

Alieleza kuwa uelekeo wa sasa ni kusambaza nguzo za zege hasa kwa maeneo yenye unyevu sambamba na maeneo yaliyo karibu na misitu pamoja na mikondo ya mito ya maji ambayo nguzo za miti huathirika kwa kiasi kikubwa haswa kwenye msimu wa mvua hivyo nguzo za zege zitakuwa msaada mkubwa katika mazingira kama hayo na  kuboresha upatikanaji wa huduma ya umeme.

“Kama mnavyofayahamu kwa sasa uelekeo ni kusambaza nguzo za zege badala ya nguzo za miti hasa katika maeneo ambayo yana asili ya unyevu, maeneo karibu na mito ya maji ama visiwa ambapo nguzo za miti huathiriwa na mazingira hayo”, aliongeza. 

Naye Mhe. Deogratius Ndejembi Waziri wa Nishati alisema kuwa ujenzi wa kiwanda hiko umekamilika mwaka huu na kuanza uzalishaji wake rasmi Februari, 2026 ambapo mpaka sasa wastani wa nguzo zinazozalishwa ni 80 hadi 120 kwa siku ambapo mpaka sasa gharama ya shilingi bilioni 6.4 imeshatumika katika hatua zote hadi uzalishaji ulipoanza ambapo kiasi cha shilingi bilioni 1.4 bado hazijalipwa kwa mkandarasi ambaye bado yupo kwenye kipindi cha uangalizi.

“Kiwanda hiki kilianza uzalishaji rasmi mwezi Februari mwaka huu ambapo kwa sasa kina uwezo wa kuzalisha nguzo 80 hadi 120, mpaka sasa ujenzi wa kiwanda hiki hadi uzalishaji ulipoanza imetumia gharama ya shilingi bilioni 6.4 ambapo bado kuna billioni 1.6 bado haijalipwa kwa mkandarasi kwa kuwa yupo kwenye kipindi cha uangalizi”, aliongeza Mhe. Ndejembi. 

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO Bw. Lazaro Twange ameeleza kuwa kukamilika kwa kiwanda hiko kunaenda kuleta mageuzi makubwa kwani nguzo za zege ni teknolojia ambayo bado inakuwa hivyo Shirika bado linaendelea kuikuza sekta  na kuwa na utoshelevu wa nguzo zenyewe kwa matumizi ya wananchi. 

“Baada ya kukamilika kwa ujenzi wa kiwanda na kuanza uzalishaji ambapo kwa hali ilivyo ya matumizi ya nguzo za zege ni teknolojia ambayo bado inakuwa hivyo kama Shirika tutahakikisha tunaisimamia sekta hii ili kuendelea kuwapatia wateja wetu huduma ya umeme wa uhakika”, alisema Bw. Twange. 

Ziara hiyo ya kamati ya kudumu ya bunge ya nishati na madini inalenga kufanya ukaguzi wa miradi mbalimbali inayotekelezwa na Shirika katika maeneo mbalimbali nchini ili kujionea ufanisi wake.





 

📍Geita.

Mwenyekiti wa Kamati ya TEITI, Balozi Wilson Masilingi, ametembelea Mgodi wa Dhahabu wa Geita Gold Mining Limited akiambatana na Menejimenti ya TEITI, kwa lengo la kujitambulisha na kufanya mazungumzo na menejimenti ya mgodi huo.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Balozi Masilingi alisema ziara hiyo imelenga kujenga na kuimarisha ushirikiano kati ya TEITI na wadau wa sekta ya uziduaji, hususan migodi mikubwa inayochangia maendeleo ya taifa.

Alisema kuwa aliteuliwa kusimamia taasisi hiyo muhimu na Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan, Rais wa Tanzania, mwezi Januari mwaka huu, hivyo anaona ni muhimu kujitambulisha kwa wadau wakuu wa sekta hiyo ili kuimarisha ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu ya TEITI.

“Utekelezaji wa shughuli za EITI nchini ni wa ushirikiano, hivyo nitashirikiana kikamilifu na wadau wote ili kuendeleza gurudumu la uwazi na uwajibikaji katika sekta ya uziduaji,” alisema Balozi Masilingi.

Katika ziara hiyo, menejimenti ya mgodi ilitoa maelezo kuhusu maendeleo yaliyofikiwa tangu kuanzishwa kwa mgodi huo, ikiwemo namna wanavyotekeleza sheria, kanuni na miongozo ya sekta ya madini pamoja na masharti ya leseni ya uchimbaji.

Aidha, ilielezwa kuwa mgodi huo umeendelea kutenga fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) katika halmashauri mbalimbali za Mkoa wa Geita, hatua inayochangia maendeleo ya jamii zinazouzunguka mgodi.

Pia ilibainishwa kuwa kwa sasa mgodi huo unaendeshwa kwa kiasi kikubwa na Watanzania na umeendelea kuongeza ajira kwa wananchi wa ndani ikilinganishwa na miaka ya awali ya uendeshaji wake.

Balozi Masilingi aliishukuru menejimenti ya mgodi kwa mapokezi mazuri waliompatia pamoja na utayari wao wa kuendeleza ushirikiano kwa manufaa ya sekta ya uziduaji na maendeleo ya taifa.

Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa TEITI, Bi. Mariam Mgaya, aliishukuru menejimenti ya mgodi kwa kuendelea kushirikiana na TEITI katika utekelezaji wa matakwa ya EITI pamoja na Sheria ya TEITA ya mwaka 2015, inayolenga kuimarisha uwazi na uwajibikaji katika sekta ya uziduaji.

Alisisitiza kuwa ushirikiano huo unapaswa kuendelezwa ili kuongeza uwazi na uwajibikaji katika usimamizi wa rasilimali za madini, mafuta na gesi asilia nchini.

Naye Meneja wa mgodi huo, Bw. Ashraf Suryaningrat, alisema Geita Gold Mining Limited itaendelea kushirikiana kikamilifu na TEITI katika kufanikisha lengo la uwazi na uwajibikaji katika sekta ya uziduaji, akibainisha kuwa mgodi huo ni miongoni mwa wadau wakubwa wa TEITI nchini.

 

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo, Mhe. Deodatus Mwanyika (Mb), ameeleza kuridhishwa kwake na hatua ya ujenzi wa jengo la kisasa la Vipimo na Viwango katika Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) jijini Dar es Salaam.

Akizungumza Machi 12, 2026, Mhe. Mwanyika amebainisha kuwa mradi huo wa ghorofa 10 umefikia asilimia 93 ya utekelezaji wake, jambo linaloashiria usimamizi madhubuti na weledi katika ukamilishaji wa Jengo Jengo hilo ili kukidhi ongezeko la wanafunzi wanaodahiliwa kila mwaka.

Vilevile, Mwenyekiti huyo ametoa rai kwa uongozi wa chuo kuendelea kutoa na kuimarisha elimu ya kati (middle-level education) katika fani za biashara hususani ujasiliamali kwa kuwa ni nyenzo adhimu kwa wahitimu wanaojiandaa kuingia kwenye soko la ajira binafsi na

Kutasaidia kuongeza hadhi ya chuo na kuchochea ari ya wanafunzi wengi zaidi kujiunga na taasisi hiyo.

Amesema kuwa uimara wa chuo unategemea ubora wa mafunzo unayoyatoa na uwezo wake wa kuzalisha wataalamu wenye ushindani katika soko la ndani na nje ya nchi.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dennis Londo (Mb), amefafanua kuwa mradi huo unatekelezwa kupitia bajeti ya Serikali ya mwaka wa fedha 2025/26 na unatarajiwa kuwa na uwezo wa kubeba zaidi ya wanafunzi 4,000 kwa wakati mmoja.

Aidha amebainisha kuwa Jengo hilo la Vipimo na Viwango litakuwa kitovu cha mafunzo ya masoko na nyanja mbalimbali za kibiashara ambazo zinahitajika kwa kiasi kikubwa kulingana na mwelekeo wa sasa wa uchumi wa viwanda.

Naye Mkuu wa Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE), Prof. Edda Lwoga, ameeleza kuwa mradi huo ulioanza Mei 25, 2023, umekuwa mhimili wa mabadiliko makubwa ya kitaaluma chuoni hapo. Alibainisha kuwa kukamilika kwa jengo hilo kutaongeza fursa za udahili kwa wanafunzi wengi wanaohitaji masomo ya biashara na ujasiriamali, ikiwemo kozi fupi ambazo zimekuwa na mahitaji makubwa kwa wadau wa sekta binafsi.


Top News