Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhe. Martin Shigela, ameiagiza Halmashauri ya Wilaya ya Bukombe kubuni na kutekeleza miradi mipya ya kuongeza mapato, badala ya kuendelea kutegemea mapato ya madini peke yake.

Ametoa maelekezo hayo wakati wa Kikao Maalum cha Baraza cha kusikiliza na kujadili Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali [CAG]kwa mwaka wa fedha unaoishia Juni 2026.

Halmashauri ya Bukombe imepongezwa kwa kufaulu kupata Hati Safi katika ukaguzi wa CAG. Hati hiyo ni alama ya juu zaidi inayothibitisha kuwa fedha za umma zimetumika kwa uwazi na kwa mujibu wa sheria.

Kwa mujibu wa ripoti ya CAG, jumla ya hoja 24 zilibuliwa kwa mwaka 2026. Kati yake, hoja 5 zimeshatekelezwa na hoja 19 zinaendelea kutekelezwa

Mkuu wa Mkoa amewataka Madiwani kuacha tabia ya "kutengeneza hoja" ili zijibiwe, na badala yake kuzuia mapungufu kabla hayajatokea ili kuitunza taswira ya Serikali.

Halmashauri hiyo imefanikiwa kukusanya Shilingi Bilioni 5 za mapato ya ndani, sawa na asilimia 136.3 ya lengo. Hatua hiyo imeipatia sifa Halmashauri hiyo kutoka kwa Katibu Tawala wa Mkoa, Bw. Mohammed Gombat.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Bukombe, Mhe. Erick Kagoma, kwa niaba ya Madiwani, amesema amepokea na atatekeleza maelekezo ya kupunguza idadi ya hoja zinazoibuliwa na CAG katika miaka ijayo.










Na Mwandishi Wetu
WAFUGAJI wa kuku nchini wamehimizwa kutumia chakula bora cha mifugo ili kuongeza uzalishaji, kuboresha afya ya kuku na kuongeza faida ya biashara zao, huku vijana wakitakiwa kuchangamkia fursa za ufugaji wa kuku kama njia ya kujiajiri na kujikwamua kiuchumi.

Wito huo unakuja sambamba na upanuzi wa huduma za kampuni ya Ekama Animal Feeds ambayo imefungua rasmi tawi jipya la Gongolamboto, Dar es Salaam, litakaloanza kutoa huduma kuanzia Julai 1, 2026 kwa lengo la kuwasogezea wafugaji bidhaa na huduma za kitaalamu.

Kupitia tawi hilo jipya lililopo eneo la Mombasa-Gongolamboto, wafugaji watapata huduma za ushauri wa kitaalamu kutoka kwa madaktari wa mifugo bila malipo pamoja na huduma za usafiri bure, hatua inayolenga kupunguza gharama na kuwawezesha kupata huduma kwa urahisi.

Akizungumza na Wadau wa sekta ya mifugo,Meneja mauzo kutoka kampuni ya Ekama Animal Feeds Irene Temba amesema matumizi ya chakula bora ni msingi wa mafanikio katika ufugaji wa kuku kwani huchangia kuku kukua kwa haraka, kuongeza uzalishaji wa mayai na kupunguza magonjwa yanayoweza kuathiri biashara ya mfugaji.

Aidha, amesema kuwa vijana wengi wana nafasi kubwa ya kufanikiwa kupitia ufugaji wa kuku kutokana na ongezeko la mahitaji ya nyama na mayai nchini, hivyo wanapaswa kutumia fursa hiyo kwa kuanzisha miradi ya kisasa yenye kuzingatia matumizi ya lishe bora kwa mifugo.

Imeelezwa kuwa sekta ya ufugaji inaweza kuwa chanzo kikubwa cha ajira na kipato kwa vijana ikiwa watawekeza katika elimu ya ufugaji, matumizi ya teknolojia na bidhaa zenye ubora zinazowezesha kupata mavuno yenye tija.

Ekama Animal Feeds imeendelea kusambaza chakula cha kuku katika maeneo mbalimbali ikiwemo Bagamoyo, Kimara Suka, Zanzibar, Kongowe na sasa Gongolamboto, hatua inayoongeza upatikanaji wa bidhaa zake kwa wafugaji wa maeneo mbalimbali.

Ufunguzi wa tawi hilo jipya unatarajiwa kuimarisha huduma kwa wafugaji wa Dar es Salaam na maeneo ya jirani, huku ukiwa chachu ya kuhamasisha vijana wengi zaidi kuingia kwenye ufugaji wa kuku kama biashara yenye uwezo wa kuchangia ukuaji wa uchumi wa mtu binafsi na Taifa kwa ujumla.
WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kutekeleza miradi ya maendeleo iliyoahidiwa katika Mkoa wa Singida, ikiwemo barabara, reli ya kisasa (SGR), uwanja wa ndege pamoja na miradi ya maji, afya na elimu kwa lengo la kuchochea maendeleo ya wananchi na kukuza uchumi wa Taifa.

Ametoa kauli hiyo leo (Jumamosi, Juni 27, 2026) alipohutubia mkutano wa hadhara uliofanyika katika Uwanja wa Maonesho wa Mandewa, wilayani Ikungi, mkoani Singida, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi mkoani humo.

Waziri Mkuu amesema Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amemtuma kuwahakikishia wananchi wa Mkoa wa Singida kuwa miradi yote ya maendeleo iliyoahidiwa itaendelea kutekelezwa hatua kwa hatua kwa kuzingatia vipaumbele vya Serikali.

"Mheshimiwa Rais amenituma niwahakikishie kwamba mambo ambayo wabunge wenu wamekuwa wakiyasema na ambayo aliwaahidi wananchi wa Singida yatakwenda kutekelezwa," amesema.

Amesema Serikali itaendelea kutekeleza miradi ya barabara ikiwemo Sabasaba–Sepuka–Ndago–Kizaga, Njia Panda–Makiungu–Mungaa–Misughaa–Ndago, Mkiwa–Itigi–Rungwa–Makongorosi, Iguguno–Nduguti–Sibiti, pamoja na Singida–Ilongero–Haydom, hatua zitakazorahisisha usafirishaji, biashara na kufungua fursa zaidi za kiuchumi katika Mkoa wa Singida na maeneo jirani.

Aidha, amesema Serikali itaendelea na utekelezaji wa reli ya kisasa (SGR) itakayofika Singida pamoja na ujenzi wa uwanja wa ndege wa kisasa utakaohudumia ndege za ukubwa mbalimbali na kuongeza fursa za uwekezaji na biashara.

Waziri Mkuu amesema kuchelewa kwa baadhi ya miradi kulitokana na uamuzi wa Serikali kuelekeza rasilimali katika kukamilisha miradi ya kimkakati ikiwemo Mradi wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere, Reli ya Kisasa (SGR) na Daraja la Kigongo–Busisi, ambayo sasa imeanza kutoa manufaa makubwa kwa Taifa.

"Tulifanya uamuzi wa kufunga mkanda ili tukamilishe miradi ya kimkakati. Leo Tanzania ina ziada ya umeme na miradi hiyo imeendelea kutoa manufaa makubwa kwa wananchi na uchumi wa Taifa," amesema.

Amesema Serikali itaendelea kuboresha huduma za maji, afya, elimu na miundombinu mingine ya kijamii sambamba na utekelezaji wa miradi hiyo ili kuongeza ustawi wa wananchi wa Mkoa wa Singida na Taifa kwa ujumla.






Na MWANDISHI WETU, Dar es Salaam


Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM - Bara) Ndg Stephen Wasira, amewataka Watanzania kuhifadhi na kuishi kulingana na urithi wa Mwalimu Julius Nyerere.

Akizungumza katika mahojiano maalumu, na ujumbe kutoka Serikali ya Angola, leo Juni 27, 2026. Wasira amemuelezea Mwalimu Nyerere kuwa kiongozi wa kipekee ambaye aliwaunganisha wananchi, alitawala kwa uadilifu mkubwa, na kuondoka madarakani bila kujilimbikizia mali.

Wasira alisema mojawapo ya sifa kuu za Mwalimu Nyerere ni uwezo wake wa kuwahamasisha Watanzania kushiriki kikamilifu katika masuala muhimu ya kitaifa badala ya kuwa watazamaji ukiwemo ulinzi wa taifa lao.

“Aliwashirikisha watu wote. Akieleza sababu ya vita, akawaambia ‘vita hii ni yetu sote.’ kila Mtu alipoona kiongozi wake anamweleza wazi hivi ndivyo ilivyotokea, hivi ndivyo tulivyoamua…basi mtu alishiriki moja kwa moja,”alisema Wasira akirejea Vita ya Kagera.

Kuhusu urithi halisi wa Nyerere, Wasira alitaja mambo mawili makuu ambayo yanapaswa kulindwa kwa umakini.

“Jambo moja tunalolikumbuka na tunalojaribu kulihifadhi kati ya aliyotuachia ni Uhuru. Pili ni Umoja. Kwa sababu Umoja hapa ni kitu tunachojivunia sana, nchi isiyo na ukabila, ambapo watu wa makabila na dini tofauti wanaishi pamoja kwa amani.” Amesema.

Alisema sehemu iliyogusa zaidi katika mazungumzo hayo yalikuwa maelezo ya Wasira kuhusu maisha ya Mwalimu Nyerere baada ya kung’atuka madarakani.

“Vizazi vijavyo vitamkumbuka Mwalimu Nyerere kama mtu aliyepigania uhuru wa nchi yake. Aliongoza nchi yake kwa miaka 24 kama Rais, na akaondoka madarakani akaenda kijijini. Akarudi kuwa mkulima mdogo. Hakuwa na pesa. Hakuwa na akaunti benki nje wala ndani ya nchi. Ni mtu wa kipekee sana,” alisema.

Aidha, alisema Mwalimu Nyerere aliamini kwamba uhuru wa Tanganyika hauwezi kuwa matunda zaidi pasipo nchi zingine za bara hilo kuwa huru.

"Mwalimu Nyerere aliamini kwamba uhuru wa Tanganyika bila uhuru wa Afrika kwamba usingekamilika mpaka nchi zote za Afrika ziwe huru.

“Alitoa mchango mkubwa wa ukombozi hasa kwa nchi za Kusini mwa Afrika, na mwisho aliamini katika umoja wa Afrika jambo ambalo hadi anaondoka duniani hakuweza kulikamilisha,” alieleza.






Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro imeanza utekelezaji wa mpango maalum wa kuboresha eneo la Endoro ili litumike kama sehemu ya utalii tiba kwa watalii pamoja na shughuli nyingine zinazohitaji utulivu.

Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro Abdul-Razaq Badru akiwa na Wakurugenzi wa Bodi katika eneo hilo lenye Maporomoko ya Maji (Water Falls), Mapango ya Tembo, Msitu, Wanyama wakubwa na maarufu kwa utalii wa kutembea (Walking Safaris)

Ameeleza kuwa kupitia fedha za Mfuko wa Maendeleo ya Utalii (TDL) eneo la Endoro linaboreshwa kwa ujenzi wa miundombinu ya kisasa ya Utalii  ili yatumike kama sehemu za utalii tiba, utafiti, utalii wa kutembea, mapumziko binafsi na kuondoa msongo wa mawazo.

“Endoro ni eneo lenye utulivu, lina kivutio cha Mapango ya Tembo na maporomoko ya maji yenye urefu wa mita 40, mamlaka imeamua kuboresha miundombinu yake ili mgeni akifika hapa na hasira aweze kupata utulivu na kurudi katika hali yake ya kawaida”,alisema kamishna Badru.

Makamu Mwenyekiti wa bodi hiyo Dkt. Harieth Mtae amepongeza jitihada hizo na kusema zitatoa fursa ya kuongezeka kwa  idadi ya watalii wanaotembelea kivutio hicho kilichopo hifadhi ya Ngorongoro.

Wakurugenzi wa bodi hiyo pia wamekagua geti la kisasa la kuingilia ndani ya hifadhi linalofanya kazi katika mfumo wa kisasa pamoja na minara ya mawasiliano ndani ya hifadhi inayolenga kuboresha huduma kwa watalii. 

















WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuwekeza katika elimu ya juu kwa kuboresha miundombinu ya kujifunzia na kufundishia ili kuandaa rasilimali watu yenye ujuzi na uwezo wa kuchangia maendeleo ya Taifa.

Ametoa kauli hiyo leo (Jumamosi, Juni 27, 2026) alipoweka jiwe la msingi la Jengo la Taaluma la Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) Kampasi ya Singida, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi mkoani Singida.

Waziri Mkuu amesema ujenzi wa jengo hilo unaakisi dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuendelea kuboresha mazingira ya elimu ya juu na kusogeza huduma hizo karibu na wananchi.

"Leo hii jengo hili la chuo chetu liko Singida. Hii ni hatua kubwa sana. Hongereni bodi, hongereni chuo, hongereni wanafunzi. Tunawatakia kila la heri," amesema.

Aidha, amewapongeza wahandisi, washauri na wakandarasi wazawa wanaotekeleza mradi huo akisema ushiriki wao unaonesha uwezo wa Watanzania katika kutekeleza miradi mikubwa ya maendeleo.

"Nimefurahishwa kwamba wahandisi wanaojenga ni wazawa, kwa sababu pia Mheshimiwa Rais alielekeza kwamba lazima tujenge uchumi unaomilikiwa na Watanzania na kujenga sekta binafsi ya ndani sambamba na uwekezaji kutoka nje," amesema.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Fedha, Mhandisi Mshamu Ali Munde, amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuipa kipaumbele sekta ya elimu kwa kuwekeza katika vyuo vya elimu ya juu ili kuongeza upatikanaji wa elimu bora, kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia, kuimarisha tafiti, ubunifu na matumizi ya teknolojia pamoja na kuzalisha wataalamu wenye ujuzi unaohitajika katika utekelezaji wa dira ya maendeleo ya Taifa.

Amesema Wizara ya Fedha itaendelea kuhakikisha rasilimali za Serikali zinaelekezwa katika miradi yenye tija kwa wananchi, ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA).

Awali, Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA), Prof. William Pallangyo, amesema jengo hilo la taaluma lina ukubwa wa mita za mraba 9,250 na litakuwa na kumbi za mafunzo, madarasa, kumbi za mihadhara, ukumbi wa mikutano pamoja na ofisi za watumishi.

Amesema mradi huo wenye thamani ya shilingi bilioni 13.5 umefikia asilimia 63 ya utekelezaji na unatarajiwa kukamilika ifikapo Septemba, 2026. Aidha, ameiomba Serikali kuendelea kuwekeza katika ujenzi wa mabweni ili kukidhi ongezeko la wanafunzi litakalotokana na kukamilika kwa mradi huo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri ya TIA, Prof. Jehovaness Aikaeli, amesema bodi itaendelea kusimamia utekelezaji wa mradi huo kwa kuzingatia thamani ya fedha na kukamilika kwa wakati, huku akieleza kuwa mradi huo utachangia kuzalisha rasilimali watu yenye ujuzi kwa maendeleo ya Mkoa wa Singida na Taifa kwa ujumla.

Naye, Mhandisi Mkazi Mshauri wa Mradi, Henry Chundu, amesema jengo hilo litakuwa na uwezo wa kuhudumia wanafunzi wapatao 3,500 kwa wakati mmoja na limejengwa kwa kuzingatia viwango vya kisasa, ikiwemo mifumo ya usalama dhidi ya moto, matumizi ya teknolojia rafiki kwa mazingira na miundombinu ya kuvuna maji ya mvua.









Benki ya Equity Bank Tanzania imeungana na wadau mbalimbali katika maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Biashara Ndogo, Ndogo na za Kati (SME Day) yaliyofanyika katika Ukumbi wa NSSF Mafao House, Ilala, Dar es Salaam, ambapo ilishiriki kama mshirika na mfadhili wa hafla hiyo iliyoandaliwa na SIDO.

Katika hafla hiyo, Equity Bank Tanzania na SIDO zilisaini Hati ya Makubaliano (MoU) ya kimkakati yenye lengo la kuwawezesha zaidi ya wajasiriamali 8,000 nchini Tanzania kupitia huduma za kifedha, mafunzo ya biashara, ushauri wa kitaalamu na uunganishaji wa masoko, ili kuimarisha ukuaji wa wa biashara ndogo na kati zinazochangia uchumi na ajira nchini 

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Bi. Theresia Aloyce Mayanie, Mkuu wa Kitengo cha Wateja Wadogo, wa Kati,  na Binafsi kutoka Equity Bank Tanzania, alisema benki hiyo itaendelea kuwa mshirika mkuu wa maendeleo ya wajasiriamali nchini kupitia suluhisho mbalimbali za kifedha. Bi. Theresia alisema: "Equity Bank tunaamini kuwa wajasiriamali ndio injini ya ukuaji wa uchumi. 

Kupitia ushirikiano wetu na SIDO, tunalenga kuwawezesha maelfu ya wafanyabiashara kupata mitaji, maarifa na fursa zitakazowasaidia kukuza biashara zao na kuboresha maisha yao.

Kwa ujumla, benki hiyo imeahidi kuendelea kushirikiana na taasisi za serikali na sekta binafsi ili kuimarisha mazingira ya biashara na kusaidia ukuaji endelevu wa wajasiriamali nchini Tanzania. @equitybanktz









Top News