Na Byera  Deus,Bukoba,

Benki ya NMB imetoa msaada wa vifaa mbalimbali vya elimu na Afya  vyenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 103.2 kwa shule za msingi ,sekondari  na zahanati mkoani Kagera  huku wakifuta simanzi kwa kutoa Viti mwendo 30 kwa watoto wenye ulemavu Mgeza Mseto 

Msaada huo umepokelewa na Mkuu wa Wilaya ya Bukoba Erasto Sima Hafla ambayo imefanyika katika shule ya msingi Mgeza mseto nakugusa vifaa kwa watoto wenye mahitaji maalumu ,kupokea viti mwendo huku Halmashauri za Bukoba,Manispaa y Bukoba,Muleba na Missenyi nao wakinufaika na  msaada ikiwa ni sehemu ya kurejesha kwa jamii na kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa wanafunzi, 

Akiwasilisha taarifa kwa niaba ya NMB, Meneja wa Kanda ya Ziwa  Faraja Ng'ingo amesema benki hiyo inaendelea kujikita katika kusaidia jamii, akibainisha kuwa hadi sasa NMB ina wateja zaidi ya milioni 8, huku tangu mwaka 2021 ikiwa imerejesha kwa jamii zaidi ya shilingi Bilioni  24 katika miradi mbalimbali bara na visiwani na Kila mwaka utenga asilimia 1 ya faida kurejesha kwenye jamii.

Alisema msaada huo unalenga kupunguza changamoto za vifaa mashuleni na kuboresha huduma za afya katika zahanati  vitu ambayo jamii inavitumia Kila siku 

Vifaaa vilivyotolea ni viti Mwendo,Madawati ,vitanda vya mabweni ,mashuka,vifaaa vya kuezekea zahanati samani mbalimbali kwa Magereza 

Mkuu wa Wilaya ya Bukoba,  Erasto Sima, aliyekuwa mgeni rasmi kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Kagera, amesema vifaa hivyo vitatumika kama ilivyokusudiwa na vitasaidia kupunguza changamoto za wanafunzi kushindwa kuhudhuria masomo kutokana na uhaba wa vifaa.

 Aidha, amewahimiza wadau na wananchi wengine kuiga mfano huo kwa kuwajali watoto wenye mahitaji maalumu hata katika matukio binafsi kama sherehe za kuzaliwa.

Kwa upande wake, Meya wa Manispaa ya Bukoba, Mheshimiwa Acton Rwankomezi, ameishukuru NMB kwa mchango huo, akieleza kuwa bado manispaa inakabiliwa na upungufu wa zaidi ya madawati 1,000na kudai kuwa  msaada uliotolewa, ukiwemo wa madawati, utasaidia kupunguza kwa kiasi kikubwa Cha  changamoto hiyo. 

Nao walimu pamoja na walezi wa watoto wenye mahitaji maalumu wamepongeza msaada huo na kuitaka jamii kuendelea kushirikiana kusaidia kundi hilo muhimu ,hasa wanafunzi wa Mgeza Mseto wenye ulemavu ambao wanakabiliwa na mahitaji maaalumu.









Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema wakati umefika kwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kuangalia fursa zaidi za ushirikiano na maendeleo kwa manufaa ya nchi hizo.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 17 Aprili 2026, alipokutana na Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Balozi Stephen Patrick Mbundi, aliyefika Ikulu kwa ajili ya kujitambulisha na kuaga rasmi.

Rais Dkt. Mwinyi amemuhakikishia Balozi Mbundi kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, kwa kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, itaendelea kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa majukumu ya pamoja ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, na kumtakia kila la heri katika utekelezaji wa majukumu yake mapya.

Aidha, amesema kuwa wakati nchi wanachama zinajipanga kuimarisha ushirikiano, ipo haja sasa ya kuangalia fursa za utekelezaji wa miradi ya pamoja.

Naye Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Balozi Stephen Patrick Mbundi, ameahidi kuwa Jumuiya hiyo itaendelea kushirikiana na kufanya kazi kwa ukaribu zaidi na Zanzibar, pamoja na kumpongeza Rais Dkt. Mwinyi kwa mafanikio na maendeleo yanayofikiwa na Zanzibar hivi sasa, ikiwemo kuimarika kwa amani.












Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, akiwa na Rais Mstaafu wa Malawi, Dkt. Lazarus Chakwera, ofisini kwake jijini Dar es Salaam Jumatano April 15, 2026, kwa mazungumzo yenye lengo la kuimarisha maridhiano ya kisiasa nchini.

RAIS Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, lamemkaribisha Rais Mstaafu wa Malawi, Dkt. Lazarus Chakwera, ofisini kwake jijini Dar es Salaam Jumatano April 15, 2026, kwa mazungumzo yenye lengo la kuimarisha maridhiano ya kisiasa nchini.

Dkt. Chakwera yupo nchini kwa ziara rasmi ya kikazi kufuatia kuteuliwa kwake kuwa Mjumbe Maalum wa Jumuiya ya Madola (Commonwealth), chini ya uongozi wa Katibu Mkuu Bi. Shirley Ayorkor Botchwey.

Aliwasili Aprili 8, 2026, amepewa jukumu la kusaidia juhudi za kidiplomasia za kupunguza mvutano wa kisiasa uliotokana na uchaguzi mkuu wa Oktoba 29, 2025.

Katika kipindi cha ziara yake, Dkt. Chakwera amekutana na wadau mbalimbali wakiwemo viongozi wa serikali, vyama vya siasa, asasi za kiraia, viongozi wa dini pamoja na wanadiplomasia.

Amekutana pia na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan na kufanya naye mazungumzo yanayo lenga kuweka msingi wa majadiliano jumuishi ya kitaifa yatakayochochea maridhiano, maboresho ya mfumo wa utawala na kudumisha utulivu wa kisiasa wa muda mrefu nchini.

Ziara hii ni sehemu ya mfumo wa “Good Offices” wa Commonwealth, unaolenga kuhamasisha mazungumzo ya faragha na suluhu za amani miongoni mwa nchi wanachama.





WIZARA ya Maliasili na Utalii imewahakikishia wawekezaji na Wadau wa michezo ushirikiano wa kutosha kuwezesha ujenzi na uboreshaji wa miundombinu ya kisasa ili kuongeza thamani ya vivutio vya utalii vilivyopo hapa nchini.

Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Utalii, Bw. Nkoba Mabula ameyasema hayo alipokutana na kuzungumza na mmiliki wa Kampuni ya Tilo World Properties Holding Limited kutoka nchini China, inayojihusisha na uwekezaji wa utoaji wa huduma za malazi ndani na nje ya hifadhi.

Bw. Mabula ameongeza kuwa wakati Tanzania ikiwa katika maandalizi ya Michuano ya AFCON 2027, Wizara inahitaji kufanya uwekezaji mkubwa kwenye maeneo ya Utalii ili kuongeza thamani katika hifadhi zake ikiwemo Hifadhi ya Taifa Serengeti, Hifadhi ya Taifa Arusha, Msitu wa Asili Pugu Kazimzumbwi, eneo la Wizara Kigamboni na Msitu wa Pande ili kuwa na vivutio vipya vya utalii hususan katika kipindi hiki ambacho Tanzania inajiandaa na Michuano ya AFCON ili kupata wageni wengi ikiwemo wachezaji maarufu wa timu za taifa.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni hiyo, Bw. Adamu Deng amesema uwekezaji huo umelenga kuanza kufanyika katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti kwa kujenga kambi ya kudumu ya watalii (Permanent Camp) yenye vyumba 50 utakaogarimu kiasi cha Dola za Marekani Million 3 na utakaokamilika ndani ya miezi nane hadi kumi na mbili.

Uboreshahi wa miundombinu ndani ya Hifadhi zilizopo hapa nchini utatoa fursa ya kufikia malengo ya Serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kufikisha idadi ya watalii milioni 8 ifikapo 2030 na kuchagiza ongezeko la pato la taifa wakati na baada ya michuano ya AFCON 2027.



Waziri Mavunde Afafanua Leseni za Utafiti Ndizo zinaibua Migodi Mikubwa, Kati

📍 Dodoma

Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, amesema Serikali inaendelea na Marekebisho ya Mfumo wa Kidigitali wa  Leseni za Utafiti wa Madini utakaosimamia hatua zote za utoaji na usimamizi wa leseni hizo.

Amesema mfumo huo utahusisha utoaji wa leseni, uwasilishaji wa taarifa za kila robo mwaka, utoaji wa hati za makosa, na hata kufutwa kwa leseni pale inapobidi bila kuhitaji uingiliaji wa moja kwa moja wa binadamu.

“Baada ya mfumo huu kukamilika, hamtaniona tena natangaza kufuta leseni. Leseni itajiondoa yenyewe kupitia mfumo huu. Mfumo utakuletea taarifa zote muhimu, utakukumbusha muda wa kuwasilisha taarifa, utatoa hati za makosa pale inapobidi, na hatimaye utafuta leseni wenyewe moja kwa moja endapo masharti hayatatekelezwa,” amesisitiza Waziri Mavunde.

Mhe. Mavunde ameyasema hayo Aprili 16, 2026, alipokuwa akizungumza katika kipindi cha Morning Trumpet kinachorushwa na runinga ya UTV. Ameongeza kuwa leseni za utafiti ni msingi muhimu wa kuibua migodi mikubwa na ya kati, na kwamba maeneo yanayoshikiliwa bila kuendelezwa yanaikosesha Serikali mapato, ajira, pamoja na fursa katika mnyororo mzima wa thamani wa Sekta ya Madini.

Ameeleza hayo kufuatia uamuzi wake wa Aprili 15, 2026, wa kuielekeza Tume ya Madini kufuta leseni 40 za utafiti wa madini zenye jumla ya eneo la kilomita za mraba 900 (sawa na hekari 188,163), baada ya wamiliki wake kushindwa kutekeleza masharti ya leseni licha ya kupewa hati za makosa.

Aidha, Waziri Mavunde amesema Serikali imejipanga kuimarisha usimamizi wa Sheria ya Madini kwa kuondoa tabia ya mazoea iliyokuwepo kwa muda mrefu, akisisitiza kuwa sekta hiyo inahitaji wawekezaji wenye dhamira ya dhati ya kuendeleza rasilimali za madini kwa manufaa ya taifa.

“Sekta ya Madini kuchangia asilimia 10.1 kwenye pato la taifa si jambo dogo. Tanzania tumepiga hatua kubwa. Fikiria kama tafiti kwenye leseni hizi zingekamilika tungekuwa na migodi mingapi mikubwa na ya kati?” amehoji.

Katika hatua nyingine, ametoa wito kwa vijana wanaopenda kuingia katika sekta ya madini kujiunga na kuanzisha vikundi rasmi ili waweze kufikiwa kwa urahisi na Serikali kupitia programu maalum ya Mining For A Brighter Tomorrow, inayolenga kuwawezesha vijana, wanawake na watu wenye ulemavu kupata leseni, mitaji na vifaa vya uchimbaji.

#MadininiMaisha&Utajiri

#Mining4Development

GEITA VIJIJINI: ZAIDI ya wananchi 700,000 kutoka kata 19 katika Mkoa wa Geita wanatarijiwa kunufaika na mradi mkubwa wa maji unaogharimu zaidi ya Sh bilioni 124 katika utekelezaji wake.

Mradi huo unatarajiwa kuanza kufanya kazi Septemba 30 mwaka huu na kuzalisha jumla ya lita milioni 45 za maji kwa siku.

Hayo yalibainishwa leo Aprili 16,2026 na Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira (GEUWASA), Mhandisi Frank Changawa mbele ya Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Kenani Kihongosi alipokagua utekelezaji wa mradi huo uliopo katika Kata ya Senga Geita Vijijini mkoani Geita.

Akizungumza baada ya kukagua mradi huo Kihongosi amesema huo ni miongoni mwa miradi ya miji 28 ambayo inatekelezwa nchi nzima na unatarajiwa kuleta mabadiliko makubwa ya kiuchumi na kijamii kwa upatikanaji wa maji safi na salama kwa ufanisi na kwa muda mrefu.

Amesema katika ilani ya Uchaguzi iliyopita, serikali iliahidi kuhakikisha huduma ya maji mijini inafikia asilimia 95 na vijijini asilimia 85, lakini mradi huo utakapokamilika, watavuka lengo hilo na kufikia upatikanaji wa maji kwa asilimia 100.

“Kwa kweli nikawa naona maajabu mengi, tumekagua miradi mingi, lakini huu ni mmoja wa miradi mikubwa sana. Hongereni sana, niwapongeze viongozi, wataalamu na wasimamizi wa mradi kwa weledi wao, mmeonesha umiliki mkubwa wa kitaaluma na kuhakikisha kazi inafanyika kwa ufanisi,” amesema Kihongosi.

Awali, akisoma taarifa ya mradi huo Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira (GEUWASA), Mhandisi Frank Changawa amesema gharama ya mradi huo ni dola milioni 53.463, na hadi sasa utekelezaji umefikia asilimia 80 ya kazi nzima ya ujenzi na miundombinu.




Farida Mangube, Morogoro

Serikali kupitia Mfuko wa Misitu Tanzania (TaFF) imeendelea kuimarisha uhifadhi wa misitu na maendeleo ya jamii kwa kutoa ruzuku zinazolenga kukuza miradi endelevu ya mazingira na uchumi wa kijani.

Hayo yamebainishwa katika ufunguzi wa mafunzo kwa wanufaika wapya wa ruzuku kwa mwaka wa fedha 2025/2026 yaliyofanyika Morogoro, yakikutanisha wanufaika, waratibu wa miradi, maafisa misitu pamoja na maafisa nyuki kutoka mikoa yote nchini.

Akizungumza katika ufunguzi wa mafunzo hayo, Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu wa TaFF, Dkt. Tuli Salum Msuya, alisema mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo wanufaika katika kusimamia na kutekeleza miradi yao kwa ufanisi, hususan katika usimamizi wa fedha za ruzuku, utekelezaji wa mikataba pamoja na uandaaji wa taarifa za maendeleo ya miradi.

Alisema Serikali chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuweka kipaumbele katika sekta ya misitu kama mhimili muhimu wa uhifadhi wa mazingira, kuongeza uzalishaji na kukuza sekta ya utalii kupitia misitu endelevu.

Kwa mwaka wa fedha 2025/2026, jumla ya miradi 137 imeidhinishwa kupatiwa ruzuku kati ya zaidi ya maombi 400 yaliyowasilishwa, ambapo miradi hiyo inatekelezwa katika wilaya zaidi ya 40 nchini.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Miradi na Mipango TaFF, Johnny Richard Mbwambo, alisema mpaka sasa TaFF imetoa shilingi bilioni 70 kuwezesha miradi ya misitu na ufugaji nyuki, hatua iliyochangia upandaji miti katika mashamba zaidi ya 290 pamoja na kuimarisha uhifadhi wa maeneo makubwa ya misitu nchini.

Mbwambo aliongeza kuwa awali baadhi ya changamoto zilijitokeza katika matumizi ya fedha na utoaji wa taarifa, hali iliyosababisha kuanzishwa kwa mafunzo kabla ya utekelezaji wa miradi ili kuongeza uwajibikaji na ufanisi.

Kwa upande wao, wanufaika wa ruzuku hiyo walisema mafunzo hayo yamewasaidia kupata uelewa mpana kuhusu usimamizi wa miradi na matumizi sahihi ya fedha za ruzuku, huku wakisisitiza umuhimu wa kufanya kazi kwa ushirikiano na kuhakikisha fedha zinatumika kwa malengo yaliyokusudiwa.

Kwa sasa, takriban vikundi 79 vinanufaika na miradi inayofadhiliwa na TaFF, ikiwemo shughuli za kilimo na ufugaji nyuki zinazochangia uhifadhi wa misitu ya asili. 







Na Mwamvua Mwinyi, Pwani, April 16, 2026
MKOA wa Pwani umejipanga kupokea Mwenge wa Uhuru Aprili 18, 2026, huku wananchi wakihimizwa kujitokeza kwa wingi katika Shule ya Msingi Mtambani, Kata ya Mapinga, wilayani Bagamoyo, ambapo mwenge huo utapokelewa ukitokea Kinondoni, jijini Dar es Salaam.

Mkuu wa Mkoa huo Abubakar Kunenge, akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake kuhusu ujio wa Mwenge wa Uhuru, alieleza mwenge utakagua, kuzindua na kuweka mawe ya msingi katika miradi mbalimbali ndani ya halmashauri tisa zilizopo katika wilaya saba.

“Sisi tumejipanga kama tulivyofanya vizuri mwaka uliopita, na mwaka huu kama kawaida yetu tumeweka miradi inayogusa maslahi ya wananchi. Haturudii miradi, na tunamshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutupatia fedha za kutosha kwa ajili ya miradi ya maendeleo,” alifafanua Kunenge.

Aliongeza kuwa mwaka uliopita mkoa huo ulipata jukumu la kuwasha Mwenge wa Uhuru kitaifa na ulifanya vizuri kwa kushika nafasi ya kwanza.

Aidha, katika tathmini ya halmashauri 184 za Tanzania Bara na Zanzibar, Chalinze ilishika nafasi ya pili, Manispaa ya Kibaha nafasi ya tatu, Bagamoyo nafasi ya tisa na Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha nafasi ya 11.

Kunenge alibainisha kuwa,lengo la Mbio za Mwenge wa Uhuru ni kuimarisha umoja, mshikamano na udugu miongoni mwa Watanzania.

Alieleza baada ya kupokelewa, Aprili 18 utapokelewa na kukimbizwa halmashauri ya Bagamoyo, Aprili 19 Chalinze, Aprili 20 Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha, Aprili 21 Manispaa ya Kibaha, Aprili 22 Mafia, Aprili 23 Kisarawe, Aprili 24 Mkuranga, Aprili 25 Kibiti, Aprili 26 Rufiji na Aprili 27 utakabidhiwa mkoani Lindi.

Kwa mwaka 2026, Mwenge wa Uhuru umebeba ujumbe wa kudumisha amani, umoja na mshikamano wa kitaifa chini ya kauli mbiu isemayo: “Tanzania ni Yetu Sote, Tushikamane kwa Pamoja Kuleta Maendeleo.”

Vilevile mbio hizo pia hubeba jumbe za kudumu zikiwemo kuimarisha mapambano dhidi ya VVU/UKIMWI, dawa za kulevya, lishe bora na vita dhidi ya rushwa.

Kutokana na umuhimu huo, aliwataka wananchi kujitokeza kwa wingi kushiriki katika shughuli za Mwenge wa Uhuru katika wilaya zote utakazopitia.

Na Mwandishi wetu
WIZARA ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imeanza kuweka utaratibu wa kutumia hazina ya maarifa na uzoefu kutoka kwa Mabalozi Wastaafu ili kuimarisha utekelezaji wa mipango mbalimbali ya kuimarisha diplomasia ya nchi.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo , amebainisha utaratibu huo leo Aprili 15, 2026, jijini Dar es Salaam wakati anafungua kikao cha mashauriano kati ya uongozi wa Wizara na Mabalozi Wastafu.

"Wizara tumeanzisha utaratibu wa kuwa na vikao vya mara kwa mara na Mabalozi Wastaafu ili kuvuna maarifa na uzoefu wao kwa lengo la kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia ili ulete nanufaa katika nyanja mbalimbali kama vile, siasa, ulinzi na usalama, uchumi, biashara, uwekezaji na utalii". Balozi Kombo alisema

Balozi Kombo ametaja mifano ya maeneo ambayo angependa Mabalozi Wastaafu wachangie maarifa na uzoefu walio kuwa nao ili maeneo hayo yaendelee kuwa na manufaa zaidi kwenye nchi.

Maeneo hayo ni pamoja na mwenendo wa ufanyaji wa biashara baina ya Tanzania na nchi nyingine, hususan zilizopo barani Afrika.

Amesema utekelezaji wa Dira 2050 ambayo inalenga uchumi wa dola bilioni moja, ni eneo lingine muhimu ambalo maarifa ya Mabalozi Wastaafu yanahitajika ili kuhakikisha utekelezaji wake unakuwa wa ufanisi.

Waziri Kombo ameongeza kuwa mabadiliko yanayoendelea duniani hususan, maendeleo ya kidigitali yanahitaji mikakati thabiti ili nchi iweze kunufaika na kuwa na mipango madhubuti ya kukabiliana na athari zake. Haya yote yanahitaji mawazo ya pamoja ili kuyaendeea kwa ufanisi.

Eneo lingine ambalo Waziri Kombo alisisitiza umuhimu wa kupata uzoefu wa Mabalozi Wastaafu ni siasa za ulimwengu ambazo zimekuwa hazitabiriki na zinasababisha madhara mbalimbali, hususan katika nchi zinazoendelea kama Tanzania.

Aidha, uzoefu wa Mabalozi Wastaafu unahitajika katika kuendeleza na kuimarisha taswira nzuri ya nchi na hasa nchi inapopewa dhamana ya majukumu ya kimataifa. Balozi Kombo alisema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika mwaka 2028 na hivyo maarifa yao ni muhimu ili kuhakikisha nchi inatekeleza jukumu hilo kwa ufanisi.

Awali, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Balozi Dkt. Samwel Shelukindo alisema Wizara inaangalia uwezekano wa kuanzisha utaratibu rasmi kupitia Ofisi ya Rais-UTUMISHI ili ushirikishwaji wa Mabalozi Wastaafu uwe unatambulika rasmi.
Na Khadija Kalili
BARAZA la Madiwani la Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha limepitisha bajeti ya Mil. 50 kwa kila Kata zitakazotumika kwa ajili ya kufungua barabara zillizoharibika na kukarabati miundombinu ya barabara zilizoharibiwa na mvua zinazoendelea kunyesha.

Fedha hizo zimepitishwa kufuatia kikao cha kikanuni na Baraza hilo lililofanyika tarehe 14, 2026 ambapo utekelezaji wake ni katika kipindi cha mwaka wa fedha 2026-2027.

Mstahiki Meya wa Manispaa ya Kibaha Dkt. Mawazo Nicas amesema kuwa awali fedha hizo zilitengwa kiasi cha Mil.30 kwa kila Kata lakini kutokana na kubaini ubovu wa barabara hizo wamelazimika kuongeza bajeti hiyo hadi kufikia Mi.50.

"Tunatambua kwamba Manispaa ya Kibaha kuna Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini (TARURA) Pamoja na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS )

lakini Manispaa tumeona ni vema kutoa fedha hizo na kuzifungua baadhi ya barabara kwa dharula ili kupunguza changamoto ya ubovu wa barabara.

Mstahiki Meya Dkt.Nicas amezitaja Kata 14 zitakazopata Mi.50 kuwa ni Mailimoja, Tumbi,Pangani, Picha ya Ndege,Kongowe, Mkuza na Tangini.

Kata zingine ni Viziwaziwa, Msangani, Kibaha,Mbwawa,Visiga,Misugusugu na Tumbi.
Dkt.Nicas amewapongeza madiwani wa Manispaa hiyo kwa kuridhia bajeti hiyo inayokwenda kutatua kero ya barabara kadhalika amempongeza Mkurugenzi wa Manispaa ya Kibaha Dkt.Rogers Shemwelekwa kwa kazi nzuri ya kukusanya mapato ambayo yanasaidia kutatua kero za wananchi.

"Wananchi wetu kilio chao kikubwa ni miundombinu barabara hizi zipo chini ya TARURA na TANROADS lakini kwa upendo wa Wataalamu na Madiwani kuwajali wananchi wake wameamua kutenga fedha hizo ambazo ni mapato ya ndani zikatumike kurekebisha maeneo korofi", amesema.

Diwani wa Kata ya Sofu Mashaka Mahande amesema kutengwa kwa fedha hizo kunakwenda kupunguza kero ya barabara ambazo nyingi zimeharibika zaidi kipindi cha mvua.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na wadau wa Sekta ya Afya pamoja na wageni mbalimbali kabla ya kufungua Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na wadau wa Sekta ya Afya pamoja na wageni mbalimbali kabla ya kufungua Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Tuzo ya Heshima ya Kibinadamu ya Upasuaji wa Ubongo kutoka kwa Rais wa Chama cha Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu Tanzania (TNS) Dkt. Othman Kiloloma kwenye hafla ya ufunguzi wa Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Tuzo ya Heshima ya Kibinadamu ya Upasuaji wa Ubongo kutoka kwa Rais wa Chama cha Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu Tanzania (TNS) Dkt. Othman Kiloloma kwenye hafla ya ufunguzi wa Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.
Wafanyakazi wa Sekta ya Afya wakiwa kwenye hafla ya ufunguzi wa Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.
Wadau wa Sekta ya Afya wakiwa kwenye hafla ya ufunguzi wa Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.


Na Said Mwishehe, Michuzi TV


MWENYEKITI wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) Deodatus Balile, amesema matukio ya waandishi wa habari kukamatwa, kupigwa na kubughudhiwa yamepungua kwa kiasi kikubwa ukilinganisha na hali ilivyokuwa huko nyuma.

Balile amesema hayo leo Aprili 16, 2026 wilayani Temeke mkoani Dar es Salaam katika ufunguzi wa Mkutano Mkuu Maalumu wa jukwaa hilo uliofanyika kwa lengo la kujadili mapendekezo ya marekebisho ya Katiba.

Akizungumzia hali ya vyombo vya habari nchini na mataifa mengine, Balile amesema kumetokea mambo mengi yakiwemo waandishi kupoteza maisha, vyombo vya habari kufungwa na kukabiliwa na hali ngumu ya kiuchumi.

“Mataifa mbalimbali duniani tumeshuhudia mambo mengi yakitokea katika miaka ya karibuni kwenye tasnia yetu ya habari.

“Waandishi 140 wamepoteza maisha kutokana na vita zinazoendelea kwa baadhi ya nchini, lakini tumeshuhudia katika vyombo vya wenzetu wamepata mtanzuko mkubwa na sasa hivi Sauti ya Amerika (VOA) haipo hewani na chaneli zake zote.

“Pia katika nchi za jirani kuna waaandishi wamezuiliwa kuingia katika nchi. Kwa Tanzania matukio ya waandishi wa habari kukamatwa, kupigwa imepungua kwa kiasi kikubwa ukilinganisha na zamani.

“Nimekuwa Rais wa Jukwaa la Wahariri la Afrika Mashariki kwa muda mrefu, na nchi ambazo ni wanachama wa jukwaa hilo wanakiri Tanzania iko vizuri, lakini ni wajibu wetu sasa kuzingatia misingi ya taaluma ya habari," amesema.

Akieleza zaidi Balile amesema kuna baadhi ya waandishi wa habari wamekuwa wakiogopa kuandika kabla ya kuzuiliwa kwa maana ya kujizuia kuandika kabla ya kuzuiwa, hivyo ametoa rai ya kuondoa woga huo huku akisisitiza kutekeleza majukumu yao kwa kufuata misingi ya taaluma.


UCHUMI WA VYOMBO VYA HABARI

Kuhusu hali ya uchumi katika vyombo vya habari amesema umekumbwa na changamoto kubwa katika mataifa mbalimbali akitolea mfano nchini Marekani ambako magazeti 3,200 yamefungwa na kuondoka sokoni.

Pia, magazeti yaliyokuwa yakipata faida ya mamilioni ya fedha sasa yanajiendesha kwa faida ndogo akitolea mfano kampuni ya Standard nchini Kenya.

“Kwa Tanzania kampuni kama New Habari iliweka historia kwa kujiondoa yenyewe sokoni. Takwimu sio nzuri sana kwa kuwa mapato yamepungua sio katika vyombo vya habari pekee, lakini hadi katika taasisi za habari na sisi Jukwaa la Habari tumekuwa na changamoto za kiuchumi na ndio maana hatujakutana kwa muda mrefu,” amesema.

Kutokana na hali hiyo ametoa rai kwa vyombo vya habari nchini kutafuta vyanzo vipya vya mapato badala ya kutegemea vilivyopo hasusan matangazo na mabaki ya magazeti.

Pamoja na hayo, kwa kipekee ametoa shukrani za dhati kwa niaba ya jukwaa hilo kwa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) kutokana na kuendelea kuliunga mkono jukwaa la Wahariri.

“Kwa kipekee tunaishukuru WCF kwa kuendelea kutuamini siku hadi siku na wamekuwa wakituwezesha kwa kiwango kikubwa kwa mfano kama walianza kutuchangia kwa sh. milioni tano wakaongeza milioni 10, milioni 15, hadi Sh. milioni 30. Kwa hiyo kwa kipekee tunaishukuru WCF kwa kuendelea kuwa nasi wakati wote.” amesisitiza.






Top News