

MichuziBlogV2
Most read Swahili blog on earth
Bonyeza play kuangalia Michuzi TV LiVE
BONYEZA PLAY KUANGALIA AZAM TV LIVE
BONYEZA KUANGALIA CHANNEL TEN LIVE


Na Janeth Raphael MichuziTv
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Prof. Riziki Shemdoe, ametoa maagizo ya kuchukuliwa hatua kwa maafisa rasilimali watu watakaobainika kusababisha ucheleweshaji wa upandishaji madaraja kwa watumishi wa umma, licha ya wahusika hao kutimiza vigezo vyote vinavyohitajika.
Prof. Shemdoe ametoa kauli hiyo leo wakati akifunga Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma jijini Dodoma, kwa niaba ya Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dkt. Moses Kusiluka.
Amesema kumekuwepo na changamoto ya baadhi ya maafisa rasilimali watu kushindwa kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi, hali inayosababisha watumishi stahiki kukosa au kucheleweshwa kupanda madaraja kupitia mifumo ya kiutumishi.
“Watumishi wanaostahili kupandishwa vyeo hawapaswi kukosa haki zao kutokana na uzembe wa kiutendaji wa mtu mmoja,” amesisitiza.
Katika hatua nyingine, Prof. Shemdoe ameeleza kuwa hata yeye binafsi aliwahi kukumbana na changamoto ya kucheleweshwa kupandishwa cheo kwa takribani mwaka mmoja kutokana na kutokukamilika kwa taratibu za kiutumishi kwa wakati.
Aidha, ameelekeza kufanyika kwa tathmini maalum kwa maafisa rasilimali watu wakuu wote waliohusika na ucheleweshaji wa upandishaji madaraja katika mwaka wa fedha 2025/2026, ili hatua stahiki zichukuliwe dhidi ya waliobainika na uzembe.
Prof. Shemdoe pia amewataka waajiri kuhakikisha wanatenga bajeti ya kushiriki Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, huku akisisitiza umuhimu wa maonesho hayo katika kuboresha utoaji huduma kwa wananchi.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora (OR-MUUUB), Bw. Juma Mkomi, amesema maadhimisho hayo ni sehemu ya utekelezaji wa azimio la Umoja wa Afrika linalolenga kuenzi Siku ya Utumishi wa Umma Barani Afrika.
Ameongeza kuwa lengo la maadhimisho hayo ni kutambua mchango wa watumishi wa umma katika maendeleo ya taifa, kuhamasisha ubunifu katika utoaji huduma, pamoja na kukusanya maoni ya wananchi kuhusu ubora wa huduma zinazotolewa na taasisi za umma.
.jpeg)
-TASAC, ZMA Zaongeza Juhudi Kutatua Changamoto za Mabaharia
Na Mwandishi Wetu ,Kigoma
Serikali imesema itaendelea kuchukua hatua za kisera na kiutendaji ili kuboresha ustawi wa mabaharia nchini, ikiwemo kulinda haki zao za ajira, kuboresha mazingira ya kazi na kuhakikisha wanapata stahiki zao kwa wakati, kutokana na mchango wao mkubwa katika kukuza uchumi wa bluu.
Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mhandisi Ali Said Bakar, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, wakati wa ufunguzi wa Maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani yaliyofanyika mkoani Kigoma.
Mhandisi Bakar alisema mabaharia ni sehemu muhimu ya maendeleo ya sekta ya usafirishaji wa majini na uchumi wa taifa kwa ujumla, hivyo ni lazima changamoto zinazowakabili zipatiwe ufumbuzi wa haraka na wa kudumu.
Alisema Serikali inatambua kuwa baadhi ya mabaharia wamekuwa wakikumbana na changamoto mbalimbali ikiwemo kunyanyaswa kazini, mishahara kutolipwa kwa wakati, ujira mdogo na ukosefu wa huduma muhimu kama bima na matibabu, hali inayohitaji usimamizi madhubuti kutoka kwa mamlaka husika.
“Maadhimisho haya yanatoa fursa ya kutafakari mchango wa mabaharia katika maendeleo ya nchi na kuonyesha dhamira ya Serikali ya kushughulikia changamoto zao kupitia sera, sheria na hatua za vitendo,” alisema.
Aidha, alizitaka taasisi zinazosimamia sekta ya usafirishaji wa majini kuhakikisha zinakuwa mstari wa mbele katika kusimamia haki za mabaharia, ikiwemo upatikanaji wa bima, huduma za afya na mazingira salama ya kazi.
Kwa upande wake, Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma, Hassan Rugwa, alisema kufanyika kwa maadhimisho hayo mkoani humo ni ishara ya kutambua mchango wa Kigoma katika usafirishaji wa majini na maendeleo ya uchumi wa bluu.
Alisema maboresho makubwa yaliyofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika miundombinu ya usafiri wa majini yameongeza kwa kiasi kikubwa usafirishaji wa mizigo kupitia njia za maji.
“Maadhimisho ya Mabaharia kwa Kigoma yameaksi sekta ya usafirishaji ya zaidi ya asilimia 70 ya mizigo kusafirishwa kwa kutumia njia za maji katika Mkoa wa Kigoma jambo ambalo limeongeza umuhimu wa mabaharia katika uchumi wa taifa,” alisema Rugwa.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Bahari Zanzibar (ZMA), Fatma Said Sandali, alisema ZMA kwa kushirikiana na Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) kuendelea kuweka mifumo bora ya uratibu na usimamizi ili kutatua changamoto zinazowakabili mabaharia.
Alisema maadhimisho hayo pia ni sehemu ya kuenzi mchango wa mabaharia waliopoteza maisha wakiwa kazini na kuonyesha mshikamano kwa familia zao.
Sandali alibainisha kuwa katika kipindi cha maadhimisho hayo, wananchi watapatiwa elimu kuhusu taaluma ya ubaharia, fursa zilizopo katika sekta ya usafirishaji wa baharini na maziwa, pamoja na umuhimu wa kuzingatia misingi ya kazi yenye utu, weledi na usalama.
Aliwataka mabaharia kuendelea kuzingatia nidhamu, uzalendo na taaluma katika kutekeleza majukumu yao, akieleza kuwa dunia ya sasa inahitaji mabaharia wenye ujuzi wa hali ya juu na weledi wa kimataifa.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TASAC, Nahodha Mussa Mandia, alisema mabaharia ni nguzo muhimu ya sekta ya usafirishaji duniani na wanastahili kupewa kipaumbele katika mipango ya maendeleo.
Alisema Serikali imeendelea kufanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya usafirishaji wa majini, ikiwemo ujenzi wa Bandari ya Kisasa ya Kalema mkoani Katavi, ambayo inatarajiwa kuongeza biashara na kuchochea ukuaji wa uchumi wa bluu nchini.
Mandia alisisitiza kuwa pamoja na kutambua mchango wa mabaharia, ni muhimu kwao kuendelea kufuata sheria, kanuni na taratibu za kazi ili kuongeza tija, usalama na ushindani wa sekta hiyo.
Maadhimisho ya Siku ya Mabaharia Duniani mwaka huu yanatarajiwa kuhusisha utoaji wa elimu katika mialo ya uvuvi, shule na maeneo mbalimbali ya jamii kwa lengo la kuongeza uelewa kuhusu mchango wa mabaharia katika maendeleo ya uchumi wa Tanzania.
Na Mwandishi Wetu, Kigoma
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), Mohamed Salum, amesema kuwa usafiri wa meli ya MV Liemba una umuhimu mkubwa kwa wananchi wanaotegemea huduma za usafiri wa majini katika ukanda wa Ziwa Tanganyika, huku akieleza kuwa meli hiyo itakuwa chachu ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii.
Salum alitoa kauli hiyo wakati alipotembelea eneo la ujenzi wa meli ya MV Liemba mjini Kigoma katika maadhimisho ya Siku ya Mabaharia yanayoendelea mkoani humo.
Amesema kuwa wananchi wengi wa maeneo yanayozunguka Ziwa Tanganyika wanategemea usafiri wa majini kwa shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi, hivyo kukamilika kwa ujenzi wa meli hiyo kutasaidia kuboresha huduma za usafiri na usafirishaji wa bidhaa.
“Meli ya MV Liemba ni muhimu kwa wananchi wetu kwa sababu inatoa huduma zinazogusa maisha ya kila siku ya watu wengi. Kukamilika kwake kutaimarisha usafiri salama na wa uhakika katika maeneo yanayohudumiwa na meli hiyo,” amesema Salum.
Aliongeza kuwa katika mkoa wa Kigoma, MV Liemba itaendelea kuwa nyenzo muhimu ya kuchochea shughuli za biashara, kuunganisha jamii na kurahisisha upatikanaji wa huduma mbalimbali za kijamii kwa wananchi wa ukanda huo.
Salum amesema uwekezaji unaofanyika katika kuboresha meli hiyo unaonesha dhamira ya Serikali ya kuimarisha sekta ya usafiri wa majini na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora zinazochangia ukuaji wa uchumi wa bluu nchini.
Ziara hiyo ni sehemu ya shughuli za Maadhimisho ya Siku ya Mabaharia ambayo yanalenga kutambua mchango wa mabaharia na wadau wa sekta ya usafiri wa majini katika maendeleo ya taifa.
Wataalamu wa afya, watafiti, viongozi wa vijana na wadau mbalimbali wa maendeleo kutoka ndani na nje ya Afrika wamekutana jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kujadili namna ya kuimarisha huduma na sera za afya kwa vijana balehe barani Afrika.
Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa na Mtandao wa ARISE kupitia Mkurugenzi Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Afya ya Umma, Dkt. Mary Mwanyika Sando, Juni 22, 2026, inaeleza kuwa Mkutano wa 2026 wa Afya ya Vijana Balehe Kusini mwa Jangwa la Sahara (CAH-SSA) pamoja na Mikutano ya Mwaka ya Mtandao wa Utafiti, Sayansi ya Utekelezaji na Elimu Afrika (ARISE), unafanyika kuanzia Juni 22 hadi 25, 2026 Jijini Dar es Salaam.


.jpeg)






Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa akizungumza kwa niaba ya Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati akifungua mkutano wa tatu wa Kimataifa wa Kimkakati wa kikanda wa Pen-Plus kuhusu kukabiliana na magonjwa yasiyoambukiza makali (ICPPA 2026) unaofanyika kwa siku gatu kuanzia leo Juni 23, 2026 katika ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa JNICC, jijini Dar es Salaam.
