Hati ya makubaliano ya mashirikiano ya kuwajengea uwezo watumishi wa umma wa  Tanzania na Kenya  imesainiwa kati ya Dkt. Ernest Francis Mabonesho, Mtendaji Mkuu na Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, na Prof. Nura Mohamed, Mkurugenzi Mkuu wa Shule ya Serikali Kenya (Kenya School of Government), mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, na Rais wa Kenya, Mhe. Dkt. William Samoei Ruto.

Hafla hiyo imefanyika  Ikulu, Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 4 Mei 2026.
Makubaliano haya yanatarajiwa kuleta maendeleo makubwa katika sekta ya utumishi wa umma kwa kuimarisha mafunzo na ufanisi wa watumishi wa umma pamoja na kupanua ushirikiano wa kiutendaji kati ya nchi mbili.

KOCHA BINGWA WA MICHEZO YA UOGELEAJI AUSTIN PILLADO ATUA DAR, KUWEKA KAMBI SIKU 10


Na Mwandishi Wetu 


Na Mwandishi Wetu, Dar es salaamHATIMAYE Kocha maarufu kutoka Marekani, Austin Pillado ambaye pia ni Naibu Kocha Mkuu wa timu ya kuogelea kutoka Chuo Washington State, ametua nchini jana Jumapili kwa ajili ya kuendesha kambi maalumu ya mafunzo ya kuogelea kwa muda wa siku 10.

Kambi hiyo inayofanyika jijini Dar es Salaam, imeandaliwa na Shule ya Kimataifa ya Monti kwa kushirikiana na Chama cha Mchezo wa Kuogelea Nchini (TSA).

Akizungumza na waandishi wa habari katika mapokezi ya kocha huyo kwenye uwanja wa Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi mkuu na Mwanzilishi wa shule hiyo ya Monti International, Fatma Fernandes alisema lengo kuu ni kuinua viwango vya vipaji vya ndani kufikia hadhi ya kimataifa.

“Hii ni siku ambayo tunaanza hatua muhimu ya kuinua michezo ya kuogelea na maendeleo ya vijana hapa nchini Tanzania.

“Kwa sababu mpango huu wa mafunzo ya kambi maalumu ya kuogelea unaendana kikamilifu na maono ya uongozi wetu wa kitaifa  kutoka kwa Rais Samia Suluhu Hassan katika kukuza vipaji vya vijana, hadi kwa Waziri Habari, Sanaa na Michezo, Paul Makonda katika kuhakikisha michezo yote inapewa nafasi ya kukua. 

“Sisi Monti International tunaamini kuogelea kunaweza kuwa nguzo muhimu ya michezo Tanzania, na sekta binafsi ina nafasi kubwa ya kuchangia katika kujenga mafanikio hayo,” amesema Fatma.

Naye Mwenyekiti wa TSA, David Mwasogye amesema ujio wa kocha huyo kutasaidia kupunguza au kuziba pengo kati ya vipaji vya ndani na viwango vya kimataifa. 

“Kwa kuwaleta makocha wa kiwango cha juu kama Austin, tunawezesha vijana wetu kupata mafunzo na uchambuzi wa kitaalamu sawa na wanariadha bora duniani,” alisema Mwasogye.

Aidha, Kocha Austin Pillado mbali na kupongeza utayari wa Watanzania kujifunza na kupokea changamoto mpya, alisema Tanzania ina vipaji vingi lakini vinahitaji kupewa fursa ya kupata mafunzo ya kiwango cha juu cha kushindana kimataifa.

“Ndiyo maana nimekuja hapa Tanzania kubadilishana uzoefu kutoka kwenye mfumo wa kimataifa wa NCAA, lengo ni kuona watoto na wakufunzi wanapata mafunzo yenye viwango sawa na wanamichezo bora duniani.

Kocha maarufu kutoka Marekani, Austin Pillado ambaye pia ni Naibu Kocha Mkuu wa timu ya kuogelea kutoka Chuo Washington State (katikati) akiwa ameshika bendera ya Tanzania sambamba na Mkurugenzi mkuu na Mwanzilishi wa shule hiyo ya Monti International, Fatma Fernandes (kushoto) na Mwenyekiti wa Chama cha Kuogelea Tanzania (TSA), David Mwasogye (kulia). Austin amekuja nchini kuongoza kambi ya siku 10 ya mafunzo maalumu ya kuogelea jijini Dar es Salaam.

Kocha maarufu kutoka Marekani, Austin Pillado ambaye pia ni Naibu Kocha Mkuu wa timu ya kuogelea kutoka Chuo Washington State na Mkurugenzi mkuu na Mwanzilishi wa shule ya Monti International, Fatma Fernandes (kushoto) wakicheza pamoja na wasanii katika mapokezi yake jijini Dar es salaam. Austin amekuja nchini kuongoza kambi ya siku 10 ya mafunzo maalumu ya kuogelea jijini Dar es Salaam. 


Na Karama Kenyunko,Michuzi TV.

SERIKALI ya Tanzania na Kenya zimesaini mikataba nane ya makubaliano yenye lengo la kuimarisha sekta mbalimbali za maendeleo katika nchi hizo mbili

Hafla ya utiaji saini mikataba hiyo imefanyika leo Mei 4, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam baina ya mawaziri na watendaji wa sekta husika, ikishuhudiwa na Rais Dkt.Samia Suluhu Hasaan na Rais wa Kenya William Ruto ambaye yupo nchini kwa ziara ya kikazi ya siku mbili.

Mkataba wa kwanza uliosainiwa ni hati ya makubaliano kuhusu ushirikiano wa uendelezaji na usimamizi wa reli kati ya serikali ya Tanzania na Kenya, na wa pili unahusu upembuzi yakinifu kwa ajili ya mradi wa ujenzi wa bomba la gesi asilia kutoka Dar es Salaam hadi Mombasa.

Mkataba wa tatu ni kuhusu usaidizi wa kisheria katika masuala ya jinai kati ya serikali hizo mbili na wa nne ni makubaliano kuhusu masuala ya kilimo kati ya Tanzania na Kenya huku wa tano ukihusu utambuzi wa vyeti vya mabaharia.

Mkataba wa sita ni hati ya makubaliano wa kuimarisha uhusiano na usimamizi wa sekta ya usafiri wa njia ya maji , mkataba wa saba ni ushirikiano kati ya taasisi ya viwango Zanzibar na shirika la viwango la Kenya.

Pia wa nane ukiwa ni hati ya makubaliano kati ya vyuo vya utumishi wa umma vya Tanzania na Kenya kuhusu kujengeana uwezo katika masuala ya utumishi wa umma ambapo mikataba hiyo minane ilielezwa kuwa ishara ya ushirikiano unaozidi kuimarika kati ya Tanzania na Kenya.

Kuhuzu ziara ya kiongozi huyo, Rais Dkt.Samia amesema kuwa ziara ya Rais Ruto imekuwa ya kiserikali na imelenga kuimarisha uhusiano kati ya Tanzania na Kenya pamoja na kujadili maendeleo na uwekezaji.

“Rais wa Kenya mara nyingi amekuwa akija Tanzania kwa shughuli mbalimbali, lakini leo amekuja kwa ziara rasmi ya kiserikali.

“Katika ziara hii tumefanya mazungumzo muda mfupi uliopita kuangalia maendeleo ya nchi zetu lakini pia tumezungumza masuala ya siasa na ulinzi na kukuza uwekezaji katika nchi zetu,” amesema Rais Dk.Samia.

Aidha, Rais Samia ameeleza kuwa wamekubaliana katika miradi ya maendeleo ikiwemo bomba la gesi pamoja na sekta ya uchukuzi na miundombinu.“Tumekubaliana pia kuhusu bomba la gesi kutoka Tanzania Dar es Salaam kuelekea Mombasa Kenya na kama mlivyoshuhudia tumesaini maelewano.

“Pia kwenye uchukuzi na miundombinu tumekubaliana kwenye reli kutoka Bandari ya Tanga itapita Kilimanjaro hadi Kenya na usafiri wa ndani ya maji katika maziwa yetu hasa Ziwa Victoria kuunganisha biashara ya Kenya na Tanzania,” amesema.







Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Dkt. William Samoei Ruto wakishuhudia utiaji saini wa Mikataba 8 ya Ushirikiano baina ya Tanzania na Kenya katika sekta mbalimbali kabla ya kuzungumza na Waandishi wa Habari, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 04 Mei, 2026. Mikataba 8 iliyosainiwa ni kuhusu masuala ya usimamizi wa Reli, upembuzi yakinifu wa mradi wa bomba la Gesi kutoka Dar es Salaam hadi Mombasa, usaidizi wa Kisheria kuhusu masuala ya jinai, masuala ya Kilimo, utambuzi wa vyeti vya Mabaharia, usimamizi wa sekta ya Usafiri kwa njia ya maji, masuala ya Viwango pamoja na kujengeana uwezo kwenye masuala ya Utumishi wa Umma.

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.
Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Rais wa Jamhuri ya Kenya
Mhe. Dkt. William Samoei Ruto mara baada ya kuwasili katika viwanja
vya Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa tarehe 04 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Dkt. William Samoei Ruto mara baada ya kuwasili katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa tarehe 04 Mei, 2026.

. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa amesimama na Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Dkt. William Samoei Ruto wakati wimbo wa Taifa ukiimbwa katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 04 Mei, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Dkt. William Samoei Ruto akikagua Gwaride lililoandaliwa kwa heshima yake na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 04 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Dkt. William Samoei Ruto akisalimiana na viongozi mbalimbali waliofika kumpokea katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 04 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Dkt. William Samoei Ruto wakati wakielekea katika ukumbi wa Kikwete kwa ajili ya mazungumzo, tarehe 04 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Dkt. William Samoei Ruto akisaini Kitabu cha Wageni mara baada ya kuwasili katika ukumbi wa Kikwete, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 04 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Dkt. William Samoei Ruto akisaini Kitabu cha Wageni mara baada ya kuwasili katika ukumbi wa Kikwete, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 04 Mei, 2026.




Na Janeth Raphael- MichuziTv

Rais wa Kenya, William Ruto, ameipongeza Serikali ya Tanzania chini ya uongozi wa Samia Suluhu Hassan kwa hatua ya kuunda tume maalum ya kuchunguza matukio ya uvunjifu wa amani yaliyojitokeza wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025.

Akizungumza mara baada ya kuwasili nchini kwa ziara ya kikazi, Rais Ruto alisema uamuzi huo unaakisi uongozi thabiti, wenye uwajibikaji na unaozingatia misingi ya kisheria katika kushughulikia changamoto za kitaifa. Alieleza kuwa kuundwa kwa tume hiyo ni ishara ya dhamira ya dhati ya serikali ya Tanzania katika kuhakikisha ukweli wa matukio unajulikana na haki inatendeka kwa wote.

Tume hiyo, inayojulikana kama Tume ya Jaji Othman Chande, inalenga kufanya uchunguzi wa kina kuhusu vurugu na matukio mengine yaliyoathiri utulivu wa nchi katika kipindi hicho nyeti cha uchaguzi. Rais Ruto alisisitiza kuwa hatua hiyo itasaidia kujenga msingi imara wa amani, uwajibikaji na maridhiano ya kitaifa.

Aidha, kiongozi huyo wa Kenya alibainisha kuwa juhudi hizo zinaungwa mkono na nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, akisisitiza umuhimu wa mshikamano wa kikanda katika kulinda amani, kuimarisha ustawi wa wananchi na kukuza uchumi wa ukanda huo.

Akirejea uzoefu wa Kenya katika vipindi vya changamoto za kisiasa, Rais Ruto alieleza imani yake kuwa Tanzania itaweza kuvuka hali hiyo na kuibuka imara zaidi. Pia aliahidi kuendeleza ushirikiano wa karibu kati ya Kenya na Tanzania katika kuimarisha utawala bora, amani na maendeleo endelevu.

Kuundwa kwa tume hiyo ni sehemu ya juhudi pana za Serikali ya Tanzania kuhakikisha matukio yote yaliyojitokeza yanachunguzwa kwa uwazi na haki, huku ikiweka msingi wa kudumu wa utulivu wa kisiasa na mshikamano wa kitaifa.




TUME Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) imemkabidhi rasmi fomu za kugombea ubunge wa jimbo la Isimani kwa Emanuela Mtatifikolo Kaganda, kwa ajili ya Uchaguzi Mdogo unaotarajiwa kufanyika Juni 1 mwaka huu.

Zoezi hilo limefanyika katika ofisi za tume zilizopo Ihemi chini ya usimamizi wa Mkurugenzi wa Uchaguzi jimbo la Isimani, Caroline Ang’weni Otieno.

Emanuela alikabidhiwa fomu hizo akisindikizwa na viongozi mbalimbali wa wilaya akiwemo Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Iringa Vijijini, Costantino Kihwele ambapo baada ya kupokea fomu, Emanuela aliwashukuru viongozi na wanachama wote kwa kujitokeza, akisisitiza kuwa ana dhamira ya kutoa mchango chanya kwa maendeleo ya jimbo la Isimani.

Katika hotuba yake, aliwatambua viongozi wa jumuiya zote za chama ikiwemo jumuiya ya wazazi, vijana na UWT, pamoja na madiwani na viongozi wa ngazi mbalimbali.

Aliweka wazi kuwa, licha ya jimbo hilo kupitia kipindi kigumu kutokana na msiba wa aliyekuwa mbunge, wananchi wamethibitisha umoja na mshikamano mkubwa.

Emanuela alitoa shukurani za pekee kwa uongozi wa chama kuanzia ngazi ya shina hadi taifa, kwa kusimamia mchakato wa uteuzi kwa haki na uwazi na alipongeza pia wagombea wenzake walioshiriki mchakato huo na kuonyesha umoja baada ya kukamilika kwa uteuzi.

Aidha, alisisitiza kuwa jimbo la Isimani tangu kuanzishwa kwake limeongozwa na kiongozi mmoja, marehemu William Vangimembe Lukuvi, ambaye alifanya kazi kubwa ya kuliletea maendeleo.

Aliahidi kuendeleza misingi ya maendeleo iliyoachwa na kiongozi huyo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Iringa Vijijini, Costantino Kihwele, alimpongeza Emanuela kwa kuteuliwa na kamati kuu kuiwakilisha CCM kwenye uchaguzi huo mdogo.

Aliwahimiza wanachama kuendelea na umoja na maandalizi ya kampeni, akieleza kuwa chama kitafanya kampeni za kidiplomasia na za ushahidi wa kazi zilizofanyika.

Kihwele pia aliwapongeza wagombea wengine waliokuwa kwenye mchakato wa awali kwa kuonyesha uzalendo na kukubali matokeo, akiahidi kuwa watashirikishwa kikamilifu katika kampeni zitakapoanza rasmi.

Viongozi na washiriki wa mkutano huo walionyesha hamasa ya pamoja, huku wakiahidi kumpa mgombea wao ushindi wa kishindo katika uchaguzi wa Juni 1.







Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi ameshiriki katika dhifa maalum ya chakula iliyoandaliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa heshima ya Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mhe. William Ruto katika Ikulu ya Magogoni, Dar es Salaam leo tarehe 04 Mei 2026.

Rais William Ruto yupo nchini kwa ziara maalum ya siku mbili kuanzia tarehe 04 hadi 05 Mei 2026, ambapo pamoja na shughuli nyingine, anatarajiwa kulihutubia Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hapo kesho, tarehe 05 Mei 2026, Jijini Dodoma.








Na Karama Kenyunko Michuzi Tv

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amesema Tanzania na Kenya zimekubaliana kuondoa vikwazo vya kibiashara visivyo vya kikodi na kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi ili kukuza biashara na uwekezaji kati ya nchi hizo mbili.

Akizungumza jijini Dar es Salaam leo Mei 04, 2026 mara baada ya mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Kenya, William Ruto, aliyewasili nchini kwa ziara ya kitaifa, Rais Samia amesema mazungumzo yao yamelenga zaidi masuala ya kiuchumi yanayogusa ustawi wa mataifa hayo.

Amesema Kamati za Pamoja za Biashara kati ya Tanzania na Kenya zitaendelea kukutana mara kwa mara kujadili changamoto za kibiashara na kuhakikisha hakuna vikwazo vipya vinavyojitokeza, hatua inayotarajiwa kurahisisha biashara ya mipakani.

Katika ziara hiyo, mikataba nane imesainiwa ikihusisha sekta za nishati, miundombinu na uchukuzi, ulinzi, TEHAMA ambapo Rais Samia ameeleza kuwa katika sekta ya nishati, nchi hizo zimekubaliana kuendelea na miradi ya kuunganisha umeme, ambapo njia moja tayari imekamilika huku maandalizi ya ujenzi wa njia ya pili yakiendelea.

Kwa upande wa miundombinu, amebainisha kuwa makubaliano yamefikiwa ya ujenzi wa bomba la gesi kutoka Dar es Salaam hadi Mombasa, pamoja na kuunganisha reli kutoka Bandari ya Tanga kupitia Kilimanjaro hadi Kenya. Pia, Kenya itaunganisha reli yake na kipande cha Reli ya Kisasa (SGR) cha Tanzania kutoka Singida.

Aidha, nchi hizo mbili zimekubaliana kuimarisha usafiri wa majini katika Ziwa Victoria ili kurahisisha biashara inayohusisha Tanzania, Kenya na Uganda.

Ziara ya Rais Ruto imeelezwa kuwa sehemu ya juhudi za kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi kati ya Tanzania na Kenya pamoja na kufungua fursa mpya za maendeleo kwa wananchi wa nchi hizo.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu Ziara ya Kitaifa ya Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Dkt. William Samoei Ruto, Ikulu Jijini, Dar es Salaam, tarehe 04 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Dkt. William Samoei Ruto akizungumza na Waandishi wa Habari kufuatia Ziara yake ya Kitaifa, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 04 Mei, 2026.


Top News