Na Mwandishi wetu- MBEYA

Serikali imeendelea kuimarisha uwezo wa Kitaifa wa Kuzuia, Kujiandaa, Kukabiliana na Kurejesha hali baada ya maafa ili kuhakikisha wananchi wanaishi katika mazingira salama ya  kuepuka madhara makubwa yatokanayo na maafa.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Tawala Msaidizi Mipango na Uratibu Ofisi ya Mkoa wa Mbeya, Dkt. Noah Sikwese wakati akifunga mafunzo kwa Wajumbe Wateule wa Timu ya Kukabiliana na Dharura (RERT), Waatalamu wa Unendeshaji wa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura (REOCC) katika Mkoa huo yaliyoandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa.

Dkt. Sikwese, amesema timu za kukabiliana na dharura zimejengewa msingi muhimu wa utendaji utakaowezesha Mkoa kuwa na uwezo wa kujiandaa na kukabiliana na matukio ya dharura kwa haraka  na ufanisi mkubwa .

“Timu hizi zitahusika katika kufanya tathmini za awali na za kina wakati wa maafa kubaini mahitaji halisi ya waathirika, pamoja na kuratibu upatikanaji wa rasilimali muhimu kwa ajili ya kukabiliana na athari za maafa,” alisema Dkt. Sikwese.

Pia, aliongeza kwamba mafunzo yamekuwa nyenzo muhimu katika kujenga na kuimarisha uwezo wa kitaalamu na kiutendaji kwa watumishi wanaohusika katika Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya dharura.

“Kuanzishwa kwa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura Mkoa wa Mbeya ni hatua muhimu katika kuimarisha uratibu wa shughuli za usimamizi wa maafa. Kituo hiki kitawezesha ufuatiliaji wa matukio  kwa ukaribu, ukusanyaji na uchambuzi wa taarifa kwa wakati, pamoja na kuimarisha mawasiliano miongoni mwa wadau,” alieleza.

Sambamba na hilo Dkt. Sikwese alifafanua kuwa, utekelezaji wa mafunzo hayo ulianza katika Mikoa a Mwanza, Arusha, Dodoma, ambapo hatua za kuanzisha Vituo vya Operesheni na Mawasiliano ya Dharura pamoja na kuimarisha Timu za kukabiliana  na maafa zilianza kutekelezwa.

“Ni matarajio yangu mafunzo haya yataongeza ufanisi, uwajibikaji, ustahimilivu dhidi ya majanga katika Mkoa wetu wa Mbeya,”aliongeza.

Aidha, alitoa wito kwa wataalamu wote waliopatiwa mafunzo kuendelea kuyafanyia kazi maarifa na stadi, kudumisha nidhamu ya kazi na kujenga utamaduani wa ushirikiano wa kitaalamu huku akiwasisitiza kuendelea kufanya mazoezi ya mara kwa mara ya uokoaji na  utoaji wa huduma ya kwanza kwa majeruhi au waliofikwa na maafa.

“Usimamizi wa maafa ni jukumu letu sote, kila mmoja ashiriki sasa na kuchukua hatua katika eneo lake ili kuokoa na kulinda maisha, mali na mazingira,” alisisitiza Dkt. Sikwese.

Ikumbukwe kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) kwa mujibu wa Sera ya Taifa ya Usimamizi wa Maafa yam waka 2004 (Toleo la 2025) pamoja na Sheria ya Usimamizi wa Maafa Na. 6 ya mwaka 202 imeipa jukumu la kuratibu masuala yote ya usimamizi wa maafa nchini.





Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) umeendelea kuonesha dhamira yake ya kupunguza pengo la kidijitali nchini kwa kutekeleza miradi mbalimbali inayolenga kuongeza upatikanaji wa huduma za mawasiliano, intaneti na kuwajengea uwezo wananchi, hususan wasichana na vijana, katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).

Hayo yameelezwa na Kaimu Mtendaji Mkuu wa UCSAF, Mhandisi Albert Richard, wakati akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya mfuko huo katika semina iliyowakutanisha waandishi wa habari na wahariri jijini Dodoma.

Akizungumza katika semina hiyo, Mhandisi Richard amesema UCSAF imefanikiwa kuwajengea uwezo wanafunzi 1,300 wa kike kutoka shule za sekondari za umma kupitia maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Msichana na TEHAMA (Girls in ICT Day), ambayo huadhimishwa kila mwaka mwezi Aprili.

Amesema kupitia maadhimisho hayo, wanafunzi hupatiwa mafunzo kuhusu matumizi sahihi ya TEHAMA, ubunifu wa kidijitali pamoja na fursa mbalimbali zilizopo katika sekta ya teknolojia, hatua inayolenga kuwahamasisha wasichana kujikita katika masomo na taaluma zinazohusiana na sayansi, teknolojia na mawasiliano.

“Lengo letu ni kupunguza pengo la ushiriki lililopo kati ya wasichana na wavulana katika sekta ya TEHAMA na kuhakikisha wasichana wanapata nafasi sawa katika ulimwengu wa kidijitali,” amesema Mhandisi Richard.

Amefafanua kuwa katika mwaka wa fedha 2025/2026, UCSAF kwa kushirikiana na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), ilifanikiwa kutoa mafunzo ya TEHAMA kwa jumla ya wasichana 440, wakiwemo wanafunzi wa shule za msingi, sekondari, vyuo, elimu ya awali pamoja na wenye ulemavu.

Mafunzo hayo yalitolewa katika vituo vya Arusha, Dar es Salaam, Dodoma, Mbeya na Zanzibar, huku yakilenga kuongeza uelewa wa matumizi ya teknolojia na kuwapa washiriki ujasiri wa kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kidijitali.

Mbali na uwezeshaji wa vijana, UCSAF pia inaendelea na utekelezaji wa mradi wa kutoa huduma za bure za intaneti katika maeneo ya wazi yenye matumizi makubwa ya wananchi, ikiwa ni sehemu ya kuongeza upatikanaji wa huduma za kidijitali kwa urahisi zaidi.

Kupitia mradi huo, vituo 17 vya intaneti ya bure vimeanzishwa katika Viwanja vya Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Sabasaba jijini Dar es Salaam. Aidha, huduma hiyo imefikishwa katika maeneo mbalimbali ikiwemo Nyerere Square na Chuo cha Informatics CIVE jijini Dodoma, Soko la Nyamagana jijini Mwanza, Kiembesamaki Zanzibar, Soko la Tabora pamoja na Lungemba Training College iliyopo Mafinga.

Kwa mujibu wa Mhandisi Richard, katika mwaka wa fedha 2024/2025 UCSAF pia ilitekeleza mradi wa intaneti ya bure katika vituo 25 vya mabasi ya mwendokasi (BRT-DART) kwa gharama ya shilingi milioni 500.

Amesema kwa mwaka wa fedha 2025/2026, utekelezaji wa mradi huo unaendelea katika maeneo 60 ya Tanzania Bara na Zanzibar, ikiwa ni jitihada za kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanapata huduma za intaneti kwa urahisi na gharama nafuu.

Katika hatua nyingine, UCSAF inaendelea kutekeleza mradi wa kuunganisha ofisi za halmashauri na mkongo wa taifa wa mawasiliano kwa njia ya faiba ili kuboresha huduma za intaneti katika taasisi za umma.

Mhandisi Richard amesema tayari utambuzi wa maeneo 10 umekamilika, huku mchakato wa manunuzi ukiendelea ili kumpata mkandarasi atakayetekeleza kazi ya kuunganisha huduma hizo pamoja na kujenga miundombinu ya kufikisha faiba katika maeneo husika.

Sambamba na hilo, UCSAF inaendelea na mradi wa kuongeza uwezo wa minara 62 ya mawasiliano kutoka teknolojia ya 2G kwenda 3G na 4G, hatua inayolenga kuboresha huduma za mawasiliano na intaneti katika maeneo ya vijijini.

Amesema kati ya minara hiyo, minara 37 inatekelezwa na kampuni ya Vodacom ambapo tayari imekamilika na imeanza kutoa huduma ya intaneti yenye kasi, huku minara 25 inayotekelezwa na TTCL ikiwa katika hatua za awali za manunuzi.

Kwa mujibu wa UCSAF, utekelezaji wa miradi hiyo unalenga kuongeza uwezo wa wananchi kupata huduma bora za mawasiliano, kukuza matumizi ya huduma za kidijitali na kuchochea shughuli za kijamii na kiuchumi kupitia teknolojia.

Aidha, miradi hiyo inatarajiwa kusaidia kuboresha huduma muhimu kama elimu mtandao, afya mtandao, biashara mtandao pamoja na huduma za kifedha kupitia simu za mkononi, hasa kwa wananchi wa maeneo ya vijijini na yasiyokuwa na huduma bora za mawasiliano.






▪️ Asema utekelezaji wa Bwawa la Farkwa kuanza baada ya kukamilika kwa taratibu za manunuzi

▪️ Aagiza kukomeshwa kwa ukamataji usio na msingi wa vitendea kazi vya wananchi

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali imejipanga kuhakikisha miradi yote ya maendeleo iliyopungua kasi ya utekelezaji inaanza tena kutekelezwa kwa kasi inayotakiwa ili wananchi waendelee kunufaika na huduma za kijamii na kiuchumi.

Amesema hayo leo Jumapili, Mei 17, 2026, alipowahutubia wananchi wa Wilaya ya Chemba katika Viwanja vya Shule ya Msingi Kambi ya Nyasa, akiwa katika ziara ya kusikiliza na kutatua changamoto za wananchi.

Dkt. Mwigulu amesema baadhi ya miradi ilipungua kasi baada ya Serikali kuelekeza nguvu kubwa katika kukamilisha miradi ya kimkakati ya kitaifa iliyokuwa imefikia hatua za mwisho, ikiwemo Mradi wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere, reli ya kisasa pamoja na Daraja la Kigongo–Busisi.

“Kilichosababisha baadhi ya miradi kupungua kasi haikuwa uzembe wala kupuuza. Ilikuwa ni mkakati wa kukamilisha miradi iliyokuwa imekaribia kukamilika ili ianze kutumika,” amesema.

Amesema Serikali sasa imeweka kipaumbele katika kuhakikisha miradi yote iliyokuwa imepungua kasi inaanza tena kutekelezwa, huku miradi ambayo mikataba yake tayari imesainiwa ikitengewa fedha za kuanza kazi.

Kuhusu Mradi wa Bwawa la Farkwa, Dkt. Mwigulu amesema mradi huo, unaokadiriwa kugharimu zaidi ya shilingi bilioni 312, utaanza kutekelezwa mara baada ya kukamilika kwa taratibu za kimanunuzi.

“Tunapoanza bajeti mpya naamini mtakuwa mmeanza kuona mkandarasi akiwa eneo la mradi kutekeleza mradi huo wa kihistoria,” amesema.

Amesema Serikali imeelekeza miradi mipya ya maji ibuniwe kwa namna itakayotoa huduma ya maji kwa matumizi ya nyumbani, mifugo na shughuli za kilimo.

Aidha, Dkt. Mwigulu amesema Serikali imeendelea kufanya uwekezaji mkubwa katika sekta za afya, elimu, maji na nishati, hatua ambayo imebadili kwa kiwango kikubwa maisha ya wananchi.

Katika sekta ya afya, amesema Serikali imejenga hospitali za wilaya zaidi ya 100, vituo vya afya zaidi ya 600 na zahanati zaidi ya 2,700, sambamba na ununuzi wa vifaa tiba vya kisasa vya uchunguzi katika hospitali za rufaa na za kanda.

Katika sekta ya elimu, amesema Serikali imejenga shule za amali 103, zikiwemo shule 29 za mkondo wa uhandisi, pamoja na kuendelea kuongeza miundombinu ya shule za msingi na sekondari nchini.

Kuhusu nishati, Dkt. Mwigulu amesema Serikali imejipanga kumaliza changamoto ya kukatika kwa umeme kupitia utekelezaji wa Mradi wa Gridi Imara wenye thamani ya zaidi ya shilingi trilioni 1.1.

“Mkiona umeme unakatika katika baadhi ya maeneo siyo upungufu wa umeme tena. Changamoto ipo kwenye uimara wa gridi kutokana na ongezeko kubwa la matumizi,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameagiza viongozi na watendaji kuacha vitendo vya ukamataji usio na msingi pamoja na kushikilia vitendea kazi vya wananchi kwa makosa madogo.

“Haya mambo ya kushikilia vitendea kazi vya wananchi tuachane nayo. Mtu anafanya shughuli yake ya kujitafutia kipato halafu mnachukua kitendea kazi chake; hiyo ni kuua mtaji na maisha ya familia yake,” amesema.

Amesema Serikali itaendelea kulinda haki za wananchi na kuhakikisha sheria hazitumiki kuwaonea wananchi au kuwanyima fursa za kufanya shughuli halali za uzalishaji.

Aidha, amesema Serikali inaendelea na hatua za kuifuta sheria ya kutaifisha mali ambayo imekuwa ikitumika vibaya katika baadhi ya maeneo na kusababisha wananchi kupoteza mali zao isivyo halali.








Na Mwandishi wetu – Dar es Salaam

Serikali imeeleza hazma yake ya kuendelea kutekeleza miradi ya mashirikiano katika sekta za kilimo na Uvuvi kwa pande mbili za Muungano ili kuongeza Ajira, uzalishaji mali, kuboresha usalama wa chakula, kuongeza thamani ya mazao, na kukuza Uchumi wa Buluu.

Hayo yameelezwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu Profesa Palamagamba Kabudi katika kikao cha ngazi ya Mawaziri cha Mashirikiano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kilichofanyika katika Ukumbi wa Mkutano wa Ofisi ya Waziri Mkuu Mtaa wa Magogoni Jijini Dar es Saalaam leo Tarehe 17 Mei 2026.

Azingumzia Programu ya kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) inayotekelezwa na pande zote Mbili za Muungano, Profesa Kabudi amesema Serikali itaimarisha ushiriki katika sekta ya uvuvi wa Bahari kuu kwa kuwezesha mashirika ya uvuvi (TAFICO) kwa Tanzania Bara na (ZAFICO) kwa upande wa Zanzibar kwa kuwezeshwa kujenga meli sita za uvuvi sambamba na ujenzi wa viwanda vya kuchakata Samaki ambapo kwa upande wa Tanzania Bara kiwanda hicho kitajengwa katika wilaya ya Kilwa Mkoani Lindi na Zanzibar katika eneo la Fungurefu.

Aidha, kwa upande wa Utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi alisema kuwa, Serikali imejiandaa kutoa taarifa ya Utekelezaji wa Ilani ya chama hicho ya nusu mwaka kwa pande zote mbili za Muungano ifikapo mwezi Julai, 2026 na taarifa ya mwaka mzima ifikapo mwezi Novemba 2026.

Kwa upande wake Waziri wa Nchi, Ofisi wa Makamu wa Pili wa Rais anayeshughulikia masuala ya Sera, Uratibu na Baraza la Wawakilishi Mhe. Hamza Hassan Juma alisema Watanzania wengi wanajishughulisha na masuala ya kilimo hivyo kikao hicho kimeweza kuzungumzia fursa zinazopatikana katika sekta hizo zinazoratibiwa na ofisi hizo na kuongeza kuwa mafanikio mengi yanategemewa kupatikana katika vikao hivi vya mashirikiano.












-Ampongeza Rais Samia kuunda Tume kuchunguza kabla na baada ya Uchaguzi Mkuu

MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara, Stephen Wasira amesema kabla ya kuanza kwa mchakato wa maridhiano ya kisiasa, ni vyema kuwabaini kuwachukulia hatua za kisheria kupitia vyombo vya haki watu waliohusika na vurugu zilizosababisha madhara vikiwamo vifo.

Amempongeza Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kuunda Tume ya Kuchunguza Vurugu za Wakati na Baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025 kwa lengo la kujua kiini cha tatizo hilo.

Wasira lieleza hayo jana alipohutubia mkutano wa hadhara Mjini Kigoma akiwa katika ziara ya kichama mkoani humo.

"Mimi sijasema jina la mtu, lakini wenye kujua hayo mambo wanajijua, waache jinai ichunguzwe kama walihusika waende kwenye vyombo vya haki na sio wengi, wanaobaki watu wema tukae tufanye nao maridhiano," alisema.

Alimpongeza Rais Samia kwa kuunda tume ya kusaidia kujua chanzo cha vurugu hizo, pia alipongeza kazi nzuri iliyofanywa na tume hiyo kufanya uchunguzi huo.

"Rais (Dk. Samia) tunamshukuru na kumpongeza sana, kwa kuunda tume ya kutusaidia kujua chanzo. Tunampongeza na tunaipongeza tume ambayo imesema katika uchunguzi wake imegundua kuna watu si wengi lakini ndio walioanza mpango ule walifadhili.

"Sasa wanasema (tume) wao hawakuwa polisi wa kuwakamata, lakini wanasema tuchunguze wale walioonekana ili tusiwe tunafuga nyoka ndani ya nyumba," alisema.

Alisema hakuna anayeshabikia matukio yenye kuumiza yaliyosababisha vifo na kwamba anayefanya hivyo hayuko sawa kiakili.

"Wanasema watu wamekufa, ni nani anafurahia kufa watu labda uwe na wewe akili yako imeharibika kama unasherehekea kufa watu. Wote tunapinga mauaji, lakini nani amesababisha, halafu wale walioko wengine kama tunawahisihisi ndio tena wanataka kutufundisha namna ya kufanya...vurugu muanzishe nyie na namna ya kumaliza mgogoro mtupe nyie, hapana," alisema.








WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuhakikisha Mradi wa Maji wa Miji 28 katika Mji wa Chemba unakamilika kwa wakati ili kuongeza upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama kwa wananchi wa Wilaya ya Chemba.

“Wilaya ya Chemba ni moja ya wilaya zenye shida ya ukame na maji, lakini pia ni wilaya za uzalishaji, kwa hiyo tunahitaji sana mradi huu ukamilike haraka,” amesema.

Waziri Mkuu amesema hayo leo Jumapili, Mei 17, 2026 wakati alipotembelea na kukagua maendeleo ya utekelezaji wa Mradi wa Maji wa Miji 28 katika Mji wa Chemba unaotekelezwa kupitia Wizara ya Maji kwa kushirikiana na Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) Wilaya ya Chemba.

Akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa mradi huo, Mkurugenzi wa Usambazaji Maji kutoka Wizara ya Maji, Eng. Charles Mafie amesema mradi huo wenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 11 unatarajiwa kuhudumia wananchi zaidi ya 18,141 wa Mji wa Chemba pamoja na vijiji vya Chemba, Chambalo, Kambi ya Nyasa, Gwandi, Paranga na Makamaka.

Amesema mradi huo umefikia asilimia 76 ya utekelezaji na unahusisha ujenzi wa visima vitatu vyenye uwezo wa kuzalisha maji lita 207,000 kwa saa, matenki ya kuhifadhi maji, kituo cha kusukuma maji pamoja na ulazaji wa mabomba ya kusambaza maji yenye urefu wa kilomita 60.

Aidha, amesema mradi huo utaongeza upatikanaji wa maji kutoka asilimia 37 ya sasa hadi asilimia 100 na kuongeza uzalishaji wa maji kutoka wastani wa lita laki moja na sabini kwa siku hadi kufikia zaidi ya lita milioni tatu kwa siku.

Mradi huo unatekelezwa na Mkandarasi M/s Megha Engineering and Infrastructure Limited (MEIL) chini ya usimamizi wa Mhandisi Mshauri WAPCOS Limited.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amewataka wakandarasi wanaotekeleza mradi huo kuhakikisha wanawalipa kwa wakati vijana, mafundi na vibarua wanaoshiriki katika utekelezaji wa kazi kupitia mikataba ya ushirikiano (subcontracting).

“Muendelee na kazi, lakini kila mnapopata fedha za mradi hakikisheni mnawalipa wanaofanya kazi pamoja nanyi. Vijana wetu waliopata subcontracting, mafundi na vibarua wote wapate malipo yao kwa wakati,” amesema.

Pia amesema Serikali imekuwa ikipokea malalamiko katika baadhi ya maeneo kuhusu miradi kukamilika huku baadhi ya watu waliohusika katika utekelezaji wake wakibaki wanadai malipo yao jambo ambalo halikubaliki.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema ana imani kubwa na usimamizi wa viongozi wa Serikali katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo akieleza kuwa usimamizi madhubuti una mchango mkubwa katika kuhakikisha miradi hiyo inaleta matokeo chanya kwa wananchi.






-Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa aridhishwa na miradi ya REA

📍Nyasa - Ruvuma

Wananchi wa Kitongoji cha Ndecha Wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma wameanza kushuhudia mwanga wa matumaini baada ya kuzinduliwa rasmi kwa mradi wa REA kwa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni 4.17 wa kusambaza umeme unaotekelezwa kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA), mradi ambao unatarajiwa kuleta mageuzi makubwa ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa eneo hilo.

Mradi huo umezinduliwa tarehe 16 Mei, 2026 na Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Ndugu  Wazo Michael Mwang’onda, ambaye amesema kuwa dhamira ya Serikali ni kuhakikisha wananchi wa vijijini wanapata huduma bora za nishati ili kuboresha maisha yao na kuchochea maendeleo ya Taifa.

Halikadhalika Bw. Mwang'onda  amewataka wananchi kutumia nafasi hiyo ya mradi kulipa shilingi 27,000 tu ili waweze kuwekewa umeme huo. 

“Tunataka kuona wananchi wanalipia 27,000 ili wawekewe umeme hata ukiuza kuku mmoja 27,000 unaenda kuweka umeme kwenye nyumba yako sio 300,000 kama ilivyokuwa hapo zamani'' amesema Kiongozi wa Mwenge kitaifa. 

Kwa upande wake, Msimamizi wa Miradi ya REA Mkoa wa Ruvuma, Mha. Hamisi  Mrope, amesema mradi wa kusambaza umeme vijijini (REDP2C) katika Wilaya ya Nyasa unalenga kufikisha huduma ya umeme katika vitongoji vyote ili kuinua maisha ya wananchi na kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Aidha, Mha. Mrope amesema mradi huo ulianza rasmi tarehe 16 Novemba 2023 na unatarajiwa kukamilika  ifikapo mwezi Oktoba, 2026, huku ukihusisha vitongoji 30, mashine umba 30 pamoja na wateja 1,247 kwa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni 4.17.

Katika Kitongoji cha Ndecha pekee, mradi umehusisha ujenzi wa kilomita 8.43 za njia ya umeme, ufungaji wa mashine umba mbili pamoja na kuunganisha wateja 94 kwa gharama ya zaidi ya shilingi milioni 307.6. Hadi sasa, miundombinu imekamilika kwa asilimia 100 huku wananchi 56 tayari wakiwa wameunganishiwa huduma ya umeme kwa gharama nafuu ya shilingi 27,000 kwa kila mteja.

Mradi huo unatekelezwa na Mkandarasi mzawa MF Electrical Engineering Ltd chini ya usimamizi wa TANESCO.

Naye, Mbunge wa jimbo  la Nyasa Mhe. John Nchimbi amesema miradi ya REA imesaidia kwa sasa vijiji vyote 84 vya wilaya Nyasa kupata huduma ya umeme huku Tanzana ikijivunia kuwa ya pili Afrika Mashariki kwa kusambaza umeme.

Kwa upande wake, Mkandarasi wa mradi huo MF Electrical Engineering Ltd mhandisi Mussa David amesema mradi huo kwa kitongoji cha Ndecha 1 wameshafikisha umeme na wameshawasha nyumba 56.

Wananchi wa Ndecha wameeleza furaha yao kutokana na ujio wa umeme ambapo mwenyekiti wa kijiji cha Linda Antony Nkoma amesema  sasa wataweza kufanya shughuli zao za kiuchumi kwa ufanisi zaidi tofauti na zamani walipotegemea taa za vibatari na vyanzo vya nishati visivyo salama.

Uzinduzi wa mradi huo umeonekana kuwa hatua muhimu katika safari ya kuwaletea wananchi maendeleo endelevu huku ukiunga mkono kaulimbiu ya Mwenge wa Uhuru 2026 isemayo:

“Tanzania ni Yetu Sote, Tushikamane kwa Pamoja Kuleta Maendeleo.”







-Wananchi kuvuna lita bilioni 21 za maji chini ya ardhi


Na Mwandishi wetu


UTAFITI uliofanywa na Bodi ya Maji ya Wami Ruvu (WRWB) umeonesha kuwepo wa maji lita bilioni 21 za maji chini ya ardhi zitakazotumika kama mbadala wakati wa kipindi cha ukosefu wa maji katika mikoa ya Dar es Salaam na Pwani.

Hatua hiyo muhimu ya WRWB ni sehemu ya utekelezaji wa awamu ya kwanza katika kutafuta vyanzo vipya mbadala vya maji katika kukabiliana na ukosefu wa mji katika mikoa ya Dar es salaam na Pwani.

Utekelezaji wa uchimbaji wa visima virefu vya maji

mbadala (back up) unatekelezwa na WRWB kwa awamu mbalimbali katika jiji la Dar es salaam na Mkoa wa Pwani kama mbadala wa maji hii ni kutokana na kuwepo kwa vipindi vya ukame jambo ambalo limekuwa likiathiri uvunaji maji katika bonde na kusababisha mgao wa maji katika maeneo ya Pwani na Dar es salaam

Aidha, uchimbaji wa awamu ya kwanza unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa Juni 2026.

Kwa mujibu wa mtaalam wa haidrojia kutoka WRWB,Omary Kizulwa alisema bodi imeamua kuwatumia wataalamu wake ili kubaini vyanzo vipya vya maji ili kuondoa kero ya maji katika mikoa ya Pwani na Dar es Salam kwa kuchimba visima mbadala vya kuhifadhi maji katika maeneo mbalimbali.

“Kwa sasa hivi Bodi ya Maji Bonde la Wami Ruvu tunafanya tafiti katika jiji la Dar es salaam na Pwani tafiti hizi zinatuwezesha kubaini maeneo ambayo yana vyanzo vya maji chini ya ardhi ili tuweze kuchimba visima” “Visima hivi vitakua kama back up (mbadala) kusaidia kipindi ambapo ukame unapotokea au ambapo hata ukame hamna viweze kutumika katika kutoa huduma ya maji” alisema“Zoezi la utafiti na uchimbaji linaendelea mpaka sasa tumeshafanya utafiti zaidi ya maeneo 40, Maeneo ya Ruvu Juu, Ruvu chini, Kigamboni , Chamazi, Ubungo, Kinondoni na Mburahati” alisema

“Tumeshafanya tafiti na tumeshaweka pointi na hivi sasa tunavyozungumza mitambo ipo site inaendelea na uchimbaji mpaka sasa zaidi ya visima 17 vimechimbwa na baadhi ya visima vimeonesha uwezo mkubwa kutoa maji na ni maji mazuri, mfano eneo la Mburahati tumechimba kisima kikubwa pale kina uwezo wa kutoa maji takribani lita elfu 50,000 mpaka 100,000 kwa saa na visima vingine kama Ilala na visima vya huku Chamazi vina karibia elfu 10,000 mpaka elfu 20,000 na kuendelea”

Aidha mtaalam huyo alisema kuwa Tanzania haina uhaba wa maji huku akibainisha kuwa maji chini ya ardhi ni lita bilioni 21 na maji juu ya ardhi ni lita bilioni 105

MRADI WA KIDUNDA

Aligusia pia mradi wa maji wa kimkakati wa Bwawa la Maji Kidunda unaotekelezwa kwa gharama ya sh.bilioni 336 kuwa utasaidia nao kuhifadhi maji ya juu ya ardhi kipindi ambapo kuna ukame

Kwa mujibu wa serikali Mradi wa Bwawa la Kidunda ni muhimu kwa kuwa utawezesha kukidhi mahitaji ya maji kwa wananchi wanaotarajiwa kuongezeka na kufikianidadi ya watu 11,387,753 ifikapo mwaka 2032, ambapo mahitaji ya maji yanakadiriwa kufikia zaidi ya lita bilioni

1.028 kwa siku. Mradi huo unatekelezwa na Mkandarasi kutoka kampuni ya Sino Hydro Corporation ya nchini China.

Bwawa la Kidunda, litakalokuwa na ujazo wa lita bilioni 190, litawezesha mitambo ya Ruvu Juu na Ruvu Chini, yenye uwezo wa kuzalisha jumla ya lita milioni 466 kwa siku, kufanya kazi katika majira yote ya mwaka na hivyo kuondoa upungufu wa maji wakati wa kiangazi.

Mitambo hiyo inahudumia zaidi ya asilimia 80 ya eneo lote la huduma la DAWASA.

Kwa upande wake wakati wa ziara ya kukagua mradi wa Kidunda msishoni mwa mwaka jana Waziri wa Maji Jumaa Aweso alisema nchi nyingi duniani kwa sasa zinakabiliwa na changamoto ya ukameinayosababishwa na mabadiliko ya tabianchi, hali ambayo pia imeanza kuathiri Tanzania.

Kutokana na hali hiyo, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, aliielekeza Wizara ya Maji kuchukua hatua za haraka na za muda mrefu ili kukabiliana na changamoto hiyo.

“Wizara ya Maji tuliweka mkakati wa muda mfupi jijini Dar es Salaam kwa kuchimba visima vitanovilivyogharimu takribani Sh.bilioni 23.6, sanjari na mkakati wa muda mrefu wa ujenzi wa Bwawa la Kidunda mkoani Morogoro pamoja na mpango wa kutumia maji ya Mto Rufiji mkoani Pwani ili kuongeza uzalishaji wa maji,” alisema

Alisema kwa sasa mahitaji ya maji kwa Jiji la Dar es Salaam ni takribani lita milioni 534 kwa siku, ilhali changamoto ya ukame ikiathiri kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa huduma ya maji.




Top News