Na Victor Masangu,Kibaha

Diwani wa kata ya Pangani Mhe. John Katele ameahidi kuchangia mifuko 10 ya simenti kwa ajili ya mradi wa ujenzi wa chuo ambacho kitakuwa kinatumika kama madrasa kinachotarajiwa kujengwa katika eneo la mtaa wa vikawe Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Mkoa wa Pwani.

Mhe. Katele ametoa ahadi hiyo wakati wa halfa fupi iliyoandaliwa maalumu kwa ajili ya kufanya mchango wa harambee kutoka kwa viongozi na wadau mbali mbali kwa lengo la kuweza kusaidia katika suala zima la kuwezesha ujenzi wa chuo hicho cha madrasa kwa watoto.

"Nashukuru nimeweza kualikwa katika halfa hii fupi nikiwa kama diwani wa kata ya Pangani na lengo langu kubwa ni kuendelea kushirikiana bega kwa bega na wananchi wangu katika mambo mbali mbali ya kijamii hususan jambo hili la ujenzi wa chuo cha madrasa na mimi nitachangia mifuko kumi ya simenti,"amebainisha Diwani Katele.

Aidha Diwani huyo amewahimiza watoto hao ambao watakuwa wanakitumia chuo hicho madrasa pindi kitakapokuja kukamailika kuweka misingi imara ya kuwa na upendo na mshikamano wa pamoja ambao utaweza kuwasaidia kufika mbali katika kujifunza mambo mbali mbali yananayohusu masuala ya dini.

Katika hatua nyingine amewaomba wadau mbali mbali na viongozi sambamba na wananchi kujitolea kwa hali na mali katika kuchangia michango mbali mbali ambayo itaweza kusaidia kukamilika kwa chuo hicho cha madrasa ambacho kinatarajiwa kujengwa katika Kata ya Pangani.




Na Janeth Raphael | Michuzi TV

Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) limetoa nafasi ya mwisho kwa vijana waliohitimu elimu ya sekondari ngazi ya Kidato cha Sita mwaka 2026 na kuchaguliwa kujiunga na mafunzo ya JKT kwa mujibu wa sheria, lakini bado hawajaripoti katika makambi waliyopangiwa.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Juni 12, 2026, jijini Dodoma na Makao Makuu ya JKT, vijana hao wametakiwa kuripoti kuanzia leo hadi Juni 15, 2026 ili kuendelea na mafunzo yao.

Taarifa hiyo imetolewa na Mkuu wa Tawi la Operesheni na Mafunzo JKT, Peter Mnyani, kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa, Rajabu Nduku Mabele.

JKT imeeleza kuwa vijana ambao hawakufanikiwa kufika katika makambi waliyoelekezwa awali wanapaswa kuripoti katika kambi za JKT zilizo karibu na maeneo wanayoishi ili kurahisisha usajili na kuendelea na mafunzo.

Hata hivyo, Jeshi hilo limefafanua kuwa utaratibu huo hauhusishi vijana wanaotakiwa kuripoti katika Kambi ya Makutupora JKT Camp, Kambi ya Ruvu JKT Camp pamoja na Kambi ya Chuo cha Uongozi Kimbiji, ambazo hazijajumuishwa katika mwongozo huo wa kuripoti kwenye kambi zilizo karibu.

JKT imewasisitiza vijana wote husika kutumia fursa hiyo ya nyongeza ya muda kuhakikisha wanaripoti ndani ya kipindi kilichotolewa ili kutimiza wajibu wao wa kujiunga na mafunzo kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizowekwa.






Na PamelaMollel, Arusha

Kampuni ya usafiri wa anga ya Pro Flight Ltd Helicopters Tanzania Kenya imeeleza dhamira yake ya kuendelea kutangaza vivutio vya utalii vya Tanzania kupitia huduma za kisasa za helikopta, hatua inayolenga kuongeza idadi ya watalii pamoja na kurahisisha usafiri katika maeneo mbalimbali ya utalii nchini

Akizungumza na vyombo vya habari jijini Arusha, Afisa wa Udhibiti wa Ubora na Usalama wa kampuni hiyo, Julius Ngeno, alisema huduma za helikopta zimekuwa nyenzo muhimu katika kuwawezesha watalii kufika kwa haraka na kwa usalama kwenye maeneo mbalimbali ya vivutio vya utalii ikiwemo Mlima Kilimanjaro, hifadhi za taifa na maeneo mengine yenye mandhari ya kipekee

Alisema Pro Flight imekuwa ikitoa uzoefu tofauti kwa wageni wanaotembelea Tanzania kwa kuwapa fursa ya kuona uzuri wa nchi kutoka angani, jambo linaloongeza thamani ya safari zao na kuwavutia zaidi kutembelea vivutio mbalimbali vya utalii.

“Tunatumia huduma za helikopta si tu kama usafiri, bali pia kama njia ya kutangaza utajiri wa vivutio vya utalii vya Tanzania. Watalii wanapata nafasi ya kuona mandhari ya kuvutia ya hifadhi, milima na maeneo mengine ya asili kwa mtazamo wa kipekee kutoka angani,” alisema Ngeno

Aliongeza kuwa kutokana na ongezeko la mahitaji ya huduma hizo, kampuni imefungua tawi jipya mkoani Kilimanjaro ili kusogeza huduma karibu zaidi na wateja na kuimarisha shughuli zake katika sekta ya utalii

Kwa mujibu wa Ngeno, huduma za Pro Flight zimekuwa zikiwanufaisha watalii wenye ratiba maalumu, wawekezaji pamoja na makundi mengine yanayohitaji usafiri wa haraka na wa uhakika katika maeneo mbalimbali nchini

Mbali na usafiri wa watalii, kampuni hiyo pia imekuwa ikitoa mchango katika shughuli za uokozi na huduma za dharura, hususan kwa wapandaji wa Mlima Kilimanjaro wanaokumbwa na changamoto za kiafya au ajali zinazohitaji msaada wa haraka.

Ngeno alisema ushiriki wa Pro Flight katika maonesho ya Karibu-KiliFair umeipa kampuni hiyo fursa ya kukutana na wadau mbalimbali wa utalii na kuonesha namna teknolojia ya usafiri wa anga inavyoweza kuchochea ukuaji wa sekta hiyo nchini.

Alisema kampuni itaendelea kushirikiana na wadau wa utalii kuhakikisha Tanzania inaendelea kujitangaza kimataifa kama moja ya destinisheni bora za utalii duniani huku ikitoa huduma za kisasa zinazokidhi mahitaji ya watalii wa kizazi cha sasa.





Na MASHAKA MHANDO -TANGA

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeomba kuendelea kwa ushirikiano kati ya Tanzania na Ireland kupitia utekelezaji wa Awamu ya Pili ya Mradi wa Maziwa Faida kuanzia mwaka 2027 hadi 2032, ili kuendeleza mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kuimarisha uzalishaji wa maziwa, kuongeza tija na kuboresha maisha ya wafugaji nchini.

Ombi hilo limetolewa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Fabian Madele, wakati akifungua rasmi Maonesho ya Ubunifu na Teknolojia katika Sekta ya Maziwa (TALIRI Open Day 2026) yaliyofanyika katika Kituo cha Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI) Kanda ya Mashariki, jijini Tanga.

Akizungumza katika hafla hiyo, Dkt. Madele amesema Mradi wa Maziwa Faida unaotekelezwa kwa ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania kupitia TALIRI na Taasisi ya Maendeleo ya Kilimo na Chakula ya Ireland (TEAGASC), kwa ufadhili wa Serikali ya Ireland kupitia Ubalozi wa Ireland nchini Tanzania, umeleta mageuzi makubwa katika sekta ya maziwa, hususani katika Mkoa wa Tanga.

Dkt. Madele amesema kabla ya kuanza kwa mradi huo, wafugaji wengi walikuwa wakizalisha wastani wa lita 3 hadi 5 za maziwa kwa ng’ombe mmoja kwa siku. Kupitia matumizi ya teknolojia bora za ufugaji, malisho bora, huduma za ugani zilizoimarishwa na mafunzo kwa wafugaji, uzalishaji umeongezeka hadi wastani wa lita 15 kwa ng’ombe mmoja kwa siku katika maeneo mengi yaliyofikiwa na mradi.

“Matokeo haya yanaonesha wazi mchango mkubwa wa utafiti, ubunifu na ushirikiano wa kimataifa katika kuongeza tija, kuboresha kipato cha wafugaji na kuimarisha usalama wa chakula na lishe nchini,” alisema Dkt. Madele.

Aidha, Dkt. Madele amesema kuwa Tanzania kwa sasa inazalisha takribani lita bilioni 4.1 za maziwa kwa mwaka, wakati mahitaji ya taifa yanakadiriwa kufikia lita bilioni 13 kwa mwaka, amesema hali hiyo inaonesha uwepo wa fursa kubwa ya kuwekeza zaidi katika uzalishaji wa maziwa ili kupunguza pengo la mahitaji na kuongeza mchango wa sekta hiyo katika uchumi wa taifa.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Balozi wa Ireland nchini Tanzania, Bi. Suzanne Keatinge, ameipongeza TALIRI kwa utekelezaji mzuri wa Mradi huo na kuwatambua watafiti, wataalamu wa ugani na wadau wote waliochangia mafanikio ya mradi huo.

Nae Mkurugenzi Mkuu wa TALIRI Prof. Erick Komba, ameishukuru Serikali ya Ireland kwa ufadhili wake na kueleza kuwa mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa Awamu ya Kwanza ya Mradi wa Maziwa Faida (2021/2022–2025/2026) yameweka msingi imara wa kuendelea kuleta mabadiliko chanya katika sekta ya maziwa nchini.

Prof. Komba alisema TALIRI itaendelea kuhakikisha kuwa matokeo ya tafiti, ubunifu na teknolojia zilizozalishwa kupitia mradi huo zinawafikia wafugaji wengi zaidi nchini kwa lengo la kuongeza uzalishaji, tija na ushindani wa sekta ya maziwa.

Aliongeza kuwa Mradi wa Maziwa Faida, uliogharimu zaidi ya Euro milioni 3 sawa na zaidi ya Shilingi bilioni 7 za Kitanzania, umenufaisha zaidi ya wanawake na vijana 3,000 katika ukanda wa pwani ya mashariki, hususan Wilaya ya Muheza mkoani Tanga.

Kwa mujibu wa Prof. Komba, mafanikio makubwa ya mradi huo ni pamoja na kufanya tafiti za malisho bora yanayostahimili mazingira ya ukanda wa pwani, kubaini aina bora za ng’ombe wa maziwa, kuwajengea uwezo maafisa ugani, kutoa mafunzo kwa wafugaji, kuimarisha vyama vya ushirika vya wafugaji, kuboresha miundombinu ya utafiti pamoja na kuanzisha mashamba darasa ambayo yamekuwa vituo muhimu vya kujifunzia na kusambaza teknolojia za kisasa za ufugaji wa ng’ombe wa maziwa.

Mradi wa Maziwa Faida unatajwa kuwa mfano bora wa ushirikiano wa maendeleo unaochochea matumizi ya utafiti na ubunifu katika kutatua changamoto za uzalishaji wa maziwa na kuchangia ukuaji endelevu wa sekta ya mifugo nchini Tanzania.









TANGA – Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeomba kuendelezwa kwa ushirikiano kati ya Tanzania na Ireland kupitia utekelezaji wa Awamu ya Pili ya Mradi wa Maziwa Faida kuanzia mwaka 2027 hadi 2032, ili kuendeleza mafanikio yaliyopatikana katika kuongeza uzalishaji wa maziwa, kuboresha tija na kuinua maisha ya wafugaji nchini.

Ombi hilo limetolewa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Fabian Madele, wakati akifungua rasmi Maonesho ya Ubunifu na Teknolojia katika Sekta ya Maziwa (TALIRI Open Day 2026) yaliyofanyika katika Kituo cha Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI) Kanda ya Mashariki, jijini Tanga.

Dkt. Madele alisema Mradi wa Maziwa Faida unaotekelezwa kwa ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania kupitia TALIRI na Taasisi ya Maendeleo ya Kilimo na Chakula ya Ireland (TEAGASC), kwa ufadhili wa Serikali ya Ireland kupitia Ubalozi wake nchini Tanzania, umeleta mabadiliko makubwa katika sekta ya maziwa, hasa Mkoa wa Tanga.

Alieleza kuwa kabla ya kuanza kwa mradi huo, wafugaji wengi walikuwa wakizalisha wastani wa lita tatu hadi tano za maziwa kwa ng’ombe mmoja kwa siku. Hata hivyo, kupitia matumizi ya teknolojia bora za ufugaji, malisho ya kisasa, huduma za ugani zilizoimarishwa pamoja na mafunzo kwa wafugaji, uzalishaji umeongezeka hadi wastani wa lita 15 kwa ng’ombe mmoja kwa siku katika maeneo mengi yaliyofikiwa na mradi.

“Matokeo haya yanaonesha wazi mchango mkubwa wa utafiti, ubunifu na ushirikiano wa kimataifa katika kuongeza tija, kuboresha kipato cha wafugaji na kuimarisha usalama wa chakula na lishe nchini,” alisema Dkt. Madele.

Aidha, alisema Tanzania kwa sasa inazalisha takribani lita bilioni 4.1 za maziwa kwa mwaka huku mahitaji ya taifa yakikadiriwa kufikia lita bilioni 13 kwa mwaka, hali inayoashiria uwepo wa fursa kubwa ya kuwekeza zaidi katika sekta ya maziwa ili kupunguza pengo la uzalishaji na kuongeza mchango wa sekta hiyo katika uchumi wa taifa.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Balozi wa Ireland nchini Tanzania, Bi. Suzanne Keatinge, aliipongeza TALIRI kwa utekelezaji mzuri wa mradi huo na kuwatambua watafiti, maafisa ugani pamoja na wadau mbalimbali waliochangia mafanikio yake.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa TALIRI, Prof. Erick Komba, aliishukuru Serikali ya Ireland kwa ufadhili wake na kueleza kuwa mafanikio yaliyopatikana katika Awamu ya Kwanza ya Mradi wa Maziwa Faida (2021/2022–2025/2026) yameweka msingi imara wa kuendelea kuleta mageuzi chanya katika sekta ya maziwa nchini.

Prof. Komba alisema TALIRI itaendelea kuhakikisha kuwa matokeo ya tafiti, ubunifu na teknolojia zilizozalishwa kupitia mradi huo zinawafikia wafugaji wengi zaidi ili kuongeza uzalishaji, tija na ushindani wa sekta ya maziwa.

Aliongeza kuwa mradi huo uliogharimu zaidi ya Euro milioni 3, sawa na zaidi ya Shilingi bilioni 7 za Kitanzania, umenufaisha zaidi ya wanawake na vijana 3,000 katika ukanda wa pwani ya mashariki, hususan Wilaya ya Muheza mkoani Tanga.

Kwa mujibu wa Prof. Komba, mafanikio mengine ya mradi huo ni pamoja na kufanya tafiti za malisho bora yanayostahimili mazingira ya ukanda wa pwani, kubaini aina bora za ng’ombe wa maziwa, kuwajengea uwezo maafisa ugani, kutoa mafunzo kwa wafugaji, kuimarisha vyama vya ushirika vya wafugaji, kuboresha miundombinu ya utafiti na kuanzisha mashamba darasa yanayotumika kusambaza teknolojia za kisasa za ufugaji.

Mradi wa Maziwa Faida umetajwa kuwa mfano wa mafanikio wa ushirikiano wa maendeleo unaochochea matumizi ya utafiti, ubunifu na teknolojia katika kutatua changamoto za uzalishaji wa maziwa na kuchangia ukuaji endelevu wa sekta ya mifugo nchini Tanzania.





Baraza la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NaCoNGO) kwa kushirikiana na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum limetangaza kuwa Jukwaa la Mwaka la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGOs) 2026 litafanyika kuanzia Oktoba 20 hadi 22, 2026 katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete jijini Dodoma.

Akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maandalizi ya jukwaa hilo, Mwenyekiti NaCoNGO Jasper Makala amesema jukwaa la mwaka huu litabeba kaulimbiu isemayo, “Fikra Mpya Kuhusu Uendelevu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali: Ubunifu, Ubia na Upatikanaji wa Rasilimali Fedha Kupitia Vyanzo vya Ndani.”

Kwa mujibu wa waandaaji, kaulimbiu hiyo inalenga kuhimiza matumizi ya ubunifu katika utendaji wa mashirika, kuimarisha ushirikiano na wadau mbalimbali pamoja na kuongeza uwezo wa mashirika kupata rasilimali kutoka ndani ya nchi ili kujenga sekta inayojitegemea na yenye uendelevu wa muda mrefu.

Jukwaa hilo linatarajiwa kuwakutanisha viongozi na watendaji wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, wawakilishi wa Serikali kutoka Wizara, Idara na Taasisi mbalimbali, Sekretarieti za Mikoa, Mamlaka za Serikali za Mitaa, Sekta Binafsi, Washirika wa Maendeleo, Taasisi za Utafiti, Vyombo vya Habari na wananchi wanaonufaika na shughuli za mashirika hayo.

Waandaaji wameeleza kuwa jukwaa hilo litatoa fursa ya kujadili mustakabali wa sekta ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali nchini, mchango wake katika maendeleo ya Taifa, pamoja na namna ya kuimarisha uwajibikaji, ubunifu na ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi sambamba na kuchangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Aidha, mjadala maalum utaangazia mikakati ya kupunguza utegemezi wa ufadhili kutoka nje kwa kuimarisha vyanzo vya ndani vya mapato, kuendeleza ubia na sekta binafsi, kutumia teknolojia za kisasa na kuimarisha mifumo ya uwazi na uwajibikaji. Washiriki pia watapata nafasi ya kuonesha mafanikio, changamoto na fursa zilizopo katika sekta hiyo.

Zaidi ya washiriki 3,000 kutoka Tanzania na nchi nyingine za ukanda wa Afrika Mashariki wanatarajiwa kushiriki katika jukwaa hilo, huku maazimio yatakayopatikana yakitarajiwa kusaidia kuimarisha mazingira wezeshi ya utendaji wa mashirika, kuongeza ushirikiano wa kimkakati na kukuza uendelevu wa sekta hiyo.

Mgeni rasmi katika Jukwaa la Taifa anatarajiwa kuwa mmoja wa viongozi wakuu wa kitaifa, huku taarifa rasmi kuhusu uthibitisho wake zikitolewa baadaye.

Kama ilivyo utaratibu, Jukwaa la Taifa litatanguliwa na majukwaa ya ngazi ya wilaya yatakayofanyika Juni na Julai 2026 pamoja na majukwaa ya ngazi ya mikoa yatakayofanyika Agosti na Septemba 2026. Majukwaa hayo yatatumika kukusanya maoni, changamoto na mapendekezo yatakayowasilishwa katika Jukwaa la Taifa.

NaCoNGO imewataka wanachama wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, taasisi za Serikali, sekta binafsi, washirika wa maendeleo, vyombo vya habari na wananchi kwa ujumla kushiriki kikamilifu katika jukwaa hilo kwa lengo la kujenga sekta imara, inayojitegemea na yenye mchango mkubwa zaidi katika maendeleo ya Tanzania.

Mashirika Yasiyo ya Kiserikali yameendelea kuwa wadau muhimu katika kuunga mkono jitihada za Serikali katika sekta mbalimbali zikiwemo elimu, afya, jinsia, uwezeshaji wa wanawake na vijana, ulinzi wa makundi maalum pamoja na ustawi wa jamii. Hivyo, Jukwaa la Mwaka la NGOs 2026 linatajwa kuwa fursa muhimu ya kutafakari mafanikio yaliyopatikana, changamoto zilizopo na mwelekeo wa baadaye wa sekta hiyo kwa kuzingatia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.




 


Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (katikati), akipozi kwa picha ya kumbukumbu na Ofisa Mkuu wa Fedha wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Bernard Tesha (kushoto), na Mkuu wa Mikakati na Data wa benki hiyo, Bw. John Mosha, ndani ya viwanja vya bunge, mara baada ya mheshimiwa waziri, kuwasilisha bajeti ya serikali ya Sh 63.2 trilioni, itakayotumika katika Mwaka 2026/2027, bungeni, jijini Dodoma, jana.

Ofisa Mkuu wa Fedha wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Bernard Tesha (kulia), Mkuu wa Mikakati na Data wa benki hiyo, Bw. John Mosha (wa tatu kulia), pamoja na baadhi ya wawakilishi kutoka taasisi za fedha, wakimsikiliza kwa makini, Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar, wakati akiwasilisha bajeti ya serikali ya Sh 63.2 trillioni, itakayotumika katika Mwaka 2026/2027, bungeni, jijini Dodoma, jana.

Ofisa Mkuu wa Fedha wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Bernard Tesha (kulia, mstari wa nyuma) na Mkuu wa Mikakati na Data wa benki hiyo, Bw. John Mosha (wa tatu kulia, mstari wa nyuma), pamoja na baadhi ya wawakilishi kutoka taasisi za fedha, wakisimama kwa utambulisho, kabla Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar, hajawasilisha bajeti ya serikali ya Mwaka 2026/2027, bungeni, jijini Dodoma, jana.

Ofisa Mkuu wa Fedha wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Bernard Tesha (wa tatu kushoto), akibadilishana mawazo na baadhi ya wawakilishi kutoka taasisi mbalimbali waliohudhuria uwasilishwaji wa bajeti ya serikali ya Mwaka 2026/2027, bungeni, jijini Dodoma, jana, uliofanywa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar.
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Ndege la Air Tanzania Company Limited (ATCL) Mhandisi Peter Ulanga (Katikati), akipiga picha ya kumbukumbu na Ofisa Mkuu wa Fedha wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Bernard Tesha (kulia kwake) na Mkuu wa Mikakati na Data wa benki hiyo, Bw. John Mosha, ndani ya viwanja vya bunge, muda mfupi baada ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar, kuwasilisha bajeti ya serikali ya Mwaka 2026/2027, bungeni, jijini Dodoma, jana.








 

MTWARA – Serikali kupitia Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora imeipongeza Taasisi ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) kwa mchango wake mkubwa wa kupunguza watumishi wasio na maadili na kuongeza tija serikalini. Pongezi hizo zimetolewa leo, Juni 11, 2026, mkoani Mtwara na Naibu Katibu Mkuu wa ofisi hiyo, Bw. Xavier Mrope Daudi, wakati akifungua rasmi Baraza la Sita la Wafanyakazi wa chuo hicho.Akizungumza katika ufunguzi huo, Bw. Daudi alisema kuwa Serikali inatambua na kuthamini juhudi kubwa zinazofanywa na chuo hicho katika kuandaa watumishi wa umma kupitia mafunzo mbalimbali. Aliongeza kuwa matunda ya kazi nzuri ya chuo hicho yameleta matokeo chanya kwa kiasi kikubwa katika kuboresha utendaji kazi na nidhamu maeneo ya kazi, jambo linalochangia kuwepo kwa watumishi wenye tija na uadilifu mkubwa.


Aidha, Naibu Katibu Mkuu alisisitiza umuhimu wa kutoa huduma bora na kutumia lugha yenye staha kwa wateja, akibainisha kuwa chuo hicho ndicho jiko linalopika watumishi wa umma tangu wanapoingia hadi wanapotoka kazini, hivyo wanapaswa kuwa mfano wa kuigwa. Alitoa rai pia kwa uongozi wa chuo kuendelea kubuni mifumo mipya ya TEHAMA kwa kushirikiana na mamlaka husika ili kurahisisha utoaji wa mafunzo kwa watumishi na jamii kwa ujumla, hasa kwa kuwa chuo hicho tayari kiko mstari wa mbele katika matumizi ya teknolojia.

Kuhusu baraza hilo la wafanyakazi, Bw. Daudi alieleza kuwa ni chombo muhimu kinachotoa fursa ya kujadiliana masuala ya tija, ufanisi, na maslahi ya watumishi. Alihimiza uwepo wa maelewano, ushirikiano, na nidhamu kazini ili kuleta mshikamano utakaosaidia chuo kupiga hatua zaidi katika nyanja za mafunzo, tafiti, na ushauri wa kitaaluma, huku akitaka majadiliano ya baraza hilo yatawaliwe na hekima, busara, na uwazi.
Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu wa TPSC, Dkt. Ernest Mabonesho, ameishukuru serikali kwa kukipatia chuo hicho jumla ya Shilingi bilioni 8.4 katika kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka wa fedha 2024/25 hadi 2026/27. Fedha hizo zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa Kampasi ya Tanga, ambapo ujenzi wake unaendelea vizuri baada ya kupokea bilioni 1.5 katika awamu ya kwanza, bilioni 2.6 awamu ya pili, na bilioni 4.3 zilizotengwa kwa ajili ya mwaka mpya wa fedha unaoanza Julai 2026.

Dkt. Mabonesho alibainisha kuwa baraza hilo la sita linajumuisha wajumbe 64 kutoka kampasi zote sita za chuo hicho, wakiwemo wawakilishi wa menejimenti, wafanyakazi, na viongozi wa chama cha wafanyakazi (TUGHE). Katika kikao hicho cha Mtwara, wajumbe watapitia na kujadili Mpango Mkakati wa Miaka Mitano (2026/27 - 2030/31), Mpango wa Bajeti ya mwaka ujao wa fedha, pamoja na tathmini ya utekelezaji wa bajeti ya kipindi kilichopita ili kuweka vipaumbele thabiti.

Alihitimisha kwa kusisitiza kuwa wafanyakazi wote wa TPSC wamejipanga kufanya kazi kwa weledi, uadilifu, na bidii ili kutekeleza kwa ufanisi malengo ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, yenye kusudi la kuleta maendeleo na kuondoa umaskini nchini.






















 


Top News