Na Karama Kenyunko Michuzi Tv

RAIS Samia Suluhu Hassan amesema Tanzania ina fursa kubwa za uwekezaji na iko tayari kuwa lango la Singapore kuingia katika masoko ya Afrika Mashariki, Ukanda wa Maziwa Makuu na Bara la Afrika kupitia Soko Huru la Afrika (AfCFTA).

Akizungumza katika Jukwaa la Biashara na Uwekezaji la Tanzania na Singapore, Rais Samia alisema Tanzania ni moja ya nchi zenye uchumi imara na unaokua kwa kasi barani Afrika, huku ikiwa na nafasi ya kimkakati inayounganisha masoko ya Afrika Mashariki, Kati na Kusini mwa Afrika.

Alisema licha ya mahusiano mazuri ya kidiplomasia kati ya Tanzania na Singapore, bado kuna fursa kubwa ambazo hazijatumika kikamilifu katika biashara na uwekezaji.

Kwa mujibu wa Rais Samia, biashara kati ya nchi hizo iliongezeka kutoka dola za Marekani milioni 74 mwaka 2020 hadi dola milioni 299 mwaka 2023 kabla ya kushuka tena hadi dola milioni 74 mwaka 2024.

Alisema tangu mwaka 1997, Singapore imesajili miradi 36 nchini Tanzania yenye thamani ya dola milioni 535 na iliyozalisha ajira 3,328.

Rais Samia alitaja maeneo yenye fursa kubwa za ushirikiano kuwa ni bandari na usafirishaji, kilimo na usindikaji wa mazao, nishati jadidifu, miundombinu janja, utalii, uchumi wa buluu, huduma za kifedha na utatuzi wa migogoro ya kibiashara.

Alisema Tanzania ni lango la biashara kwa nchi sita zisizo na bandari ambazo ni Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Malawi, Rwanda, Uganda na Zambia, huku Bandari ya Dar es Salaam ikihudumia sehemu kubwa ya biashara hiyo.

Kwa upande wake, Rais wa Singapore, Tharman Shanmugaratnam, alisema Tanzania ni nchi yenye idadi kubwa ya vijana, rasilimali nyingi za asili, fursa zinazoongezeka za uwekezaji na nafasi ya kimkakati inayounganisha masoko ya kikanda na ya kimataifa.

Alisema ushirikiano kati ya Tanzania na Singapore unaweza kuunganisha uzoefu wa Singapore katika usimamizi wa mifumo yenye ufanisi, huduma za thamani ya juu, uchumi wa kidijitali na usimamizi wa minyororo ya ugavi na hivyo kuzalisha ajira, kuongeza ujuzi na kukuza ukuaji jumuishi wa uchumi.

Rais Samia aliwataka wafanyabiashara na taasisi za pande zote mbili kutumia jukwaa hilo kujenga ushirikiano wa kudumu utakaozalisha uwekezaji, biashara na miradi yenye manufaa kwa wananchi wa nchi hizo mbili.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 09 Juni, 2026.
Na Karama Kenyunko Michuzi Tv

TANZANIA na Singapore zimefungua ukurasa mpya wa ushirikiano baada ya kusaini mikataba mitano na hati za makubaliano katika sekta mbalimbali hatua inayolenga kuimarisha biashara, uwekezaji na ushirikiano wa kiuchumi kati ya nchi hizo mbili.

Mikataba iliyosainiwa inahusi kuondoa kodi Mara mbili (Double Taxation) muendelezaji wa ujuzi, biashara za kaboni, mashauriano ya kidiplomasia na uwezeshaji wa biashara.

Mikataba hiyo itapunguza gharama za kufanya biashara, kupunguza vihatarishi vinavyotazamwa na wawekezaji na kuongeza imani kwa wawekezaji wanaotaka kuwekeza katika nchi hizo mbili.

Amesema nchi hizo pia zinaendelea kufanya kazi kuelekea mfumo wa pamoja wa utekelezaji wa biashara ya kaboni chini ya Kifungu cha sita cha Mkataba wa Paris huku zikihamasisha maendeleo endelevu.

Akizungumza katika Jukwaa la Biashara na Uwekezaji la Tanzania na Singapore jijini Dar es Salaam, Rais Tharman amesema dunia inakabiliwa na mazingira mapya ya biashara yenye kutokuwa na uhakika, hivyo kuna umuhimu wa kujenga njia mpya za ushirikiano wa kiuchumi na minyororo imara ya ugavi.

Kwa upande wake, Rais Samia Suluhu Hassan amesema yeye na Rais Tharman walifanya mazungumzo yaliyowezesha kusainiwa kwa makubaliano na hati za ushirikiano kwa manufaa ya nchi hizo mbili.

Amesema hatua hiyo inaonyesha dhamira ya pande zote mbili kuharakisha utekelezaji wa makubaliano yaliyofikiwa na kuinua uhusiano wa Tanzania na Singapore katika viwango vya juu zaidi.

Rais Samia amesema ziara hiyo ya Rais wa Singapore imekuja wakati nchi hizo zikiadhimisha miaka 45 ya uhusiano wa kidiplomasia na kwamba ni mara ya kwanza katika historia Rais wa Singapore kufanya ziara ya kiserikali nchini Tanzania.

Amesema Tanzania na Singapore zinaendelea kufurahia uhusiano mzuri unaojengwa katika misingi ya kuaminiana, ushirikiano na manufaa ya pamoja.

Na hii ni habari ya pili kuhusu fursa za biashara na uwekezaji.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongoza Ujumbe wa Tanzania kwenye mazungumzo na Ujumbe wa Singapore uliongozwa na Rais wa Nchi hiyo Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam, tarehe 09 Juni, 2026.

Viongozi hao wawili wamefanya mazungumzo rasmi yaliolenga kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Singapore katika maeneo mbalimbali hususani biashara, uwekezaji, maendeleo ya rasilimali watu na ujuzi, pamoja na uchumi wa kidijitali.Mazungumzo hayo yalifuatiwa na utiaji saini wa mikataba na Hati za ushirikiano kati ya nchi hizo mbili, na mkutano wa pamoja na waandishi wa habari.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam kwenye mkutano na Waandishi wa Habari uliofanyika, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 09 Juni, 2026.



Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Alimwoni Chaula, amefanya ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa Barabara ya Kidia, ambayo ni miongoni mwa barabara zinazoboreshwa kwa kiwango cha lami katikati ya Jiji la Dodoma.

Ujenzi wa barabara hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mh. Dk. Samia Suluhu Hassan, ya kutaka halmashauri za majiji kutenga asilimia 10 ya mapato ya ndani kwa ajili ya ujenzi na uboreshaji wa barabara za mitaa.

Akizungumza wakati wa ukaguzi huo, Mstahiki Meya Chaula aliwataka wananchi kushiriki katika kutunza miundombinu hiyo ili iweze kudumu na kuendelea kutoa huduma kwa muda mrefu.

“Wananchi kwa pamoja tunapaswa kushirikiana katika kuzitunza barabara hizi kwa kufuata taratibu zilizowekwa,Wafanyabiashara waepuke kufanya biashara katika maeneo ya barabarani kwani hali hiyo huchangia uharibifu wa miundombinu hiyo” alisema Chaula.

Aliongeza kuwa halmashauri itaendelea kutoa elimu kwa wafanyabiashara kupitia viongozi mbalimbali wa maeneo husika kuhusu athari za kufanya shughuli za biashara kwenye hifadhi ya barabara.

Kwa upande wake, mfanyabiashara wa eneo hilo, Peter Moshi ameishukuru serikali kwa kutekeleza mradi huo akisema kuwa wananchi walikuwa wakisubiri kwa muda mrefu kuona barabara hiyo ikiboreshwa na kukamilika kwake kutarahisisha shughuli za biashara, kuongeza usafiri wa uhakika na kuchochea maendeleo ya kiuchumi kwa wakazi wa eneo hilo na maeneo jirani.

Barabara zinazotekelezwa katika mpango huo zina jumla ya urefu wa kilometa moja kila moja na zinagharimu takribani shilingi bilioni 1.9 kwa ujumla.







Na Janeth Raphael MichuziTv 


Tanzania na Singapore zimekubaliana kuimarisha na kupanua ushirikiano wao katika nyanja za uchumi, biashara na uwekezaji, katika hatua inayolenga kuongeza tija na manufaa kwa wananchi wa mataifa hayo mawili.

Makubaliano hayo yamefikiwa kufuatia mazungumzo rasmi kati ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, na Rais wa Jamhuri ya Singapore, Tharman Shanmugaratnam, ambaye yupo nchini kwa ziara ya kitaifa ya kihistoria.

Akizungumza leo Jumanne, Juni 09, 2026, baada ya kumpokea mgeni huyo Ikulu, Rais Samia amesema mazungumzo yao yamejikita katika namna bora ya kuimarisha ushirikiano uliopo ili ulete matokeo halisi katika maendeleo ya pande zote mbili.

Amebainisha kuwa licha ya kuwepo kwa ukuaji wa mahusiano ya kibiashara, bado kiwango cha biashara kati ya Tanzania na Singapore hakijafikia matarajio ya nchi hizo. Kwa sasa, biashara kati ya mataifa hayo inakadiriwa kufikia takribani dola za Marekani milioni 299, huku Singapore ikiwa tayari imewekeza kupitia miradi 36 nchini Tanzania.

Rais Samia amesema makubaliano mapya yanalenga kuongeza mtiririko wa biashara, kuvutia uwekezaji zaidi, na kufungua fursa mpya katika sekta mbalimbali muhimu za kiuchumi.

Katika upande wa diplomasia, Tanzania imeiomba Singapore kufungua ubalozi wake nchini, hatua inayotarajiwa kuimarisha zaidi mahusiano ya kidiplomasia na kiuchumi kati ya nchi hizo.

Aidha, viongozi hao wamekubaliana kuanzisha mfumo wa mashauriano ya mara kwa mara utakaosaidia kuratibu mipango ya maendeleo na kushughulikia changamoto zinazoweza kujitokeza katika utekelezaji wa miradi ya ushirikiano.

Katika sekta ya kilimo, Tanzania imeonesha dhamira ya kushirikiana na Singapore katika kuimarisha usalama wa chakula, hatua itakayosaidia kuongeza biashara ya mazao ya chakula pamoja na kuhakikisha upatikanaji wa chakula cha kutosha na cha uhakika kwa pande zote mbili.

Rais Samia pia amesisitiza umuhimu wa kuwawezesha vijana, akibainisha kuwa Dira ya Taifa 2050 imeweka msingi mkubwa wa kuwajenga vijana kama nguzo ya maendeleo ya taifa katika miaka ijayo.

Ziara ya Rais Tharman Shanmugaratnam imeelezwa kuandika ukurasa mpya katika historia ya mahusiano ya Tanzania na Singapore, ikiwa ni mara ya kwanza kwa Rais wa Singapore kufanya ziara ya kitaifa nchini Tanzania tangu kuanzishwa kwa uhusiano wa kidiplomasia kati ya mataifa hayo mawili.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 09 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongoza Ujumbe wa Tanzania kwenye mazungumzo na Ujumbe wa Singapore uliongozwa na Rais wa Nchi hiyo Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam, tarehe 09 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu Ziara ya Kikazi ya Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 09 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam akizungumza na Waandishi wa Habari kufuatia Ziara yake ya Kitaifa Jijini Dar es Salaam, tarehe 09 Juni, 2026.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 09 Juni, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam, ambaye amewasili nchini kwa ziara ya Kitaifa ya siku 3, kufuatia mwaliko wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na mwenyeji wake mara baada ya kuwasili ikulu.

Mheshimiwa Rais Tharman Shanmugaratnam ameweka historia ya kuwa Rais wa kwanza kutembelea nchini tangu kuanzishwa kwa mahusiano ya kidiplomasia mwaka 1980.







Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuiimarisha mifumo ya usimamizi wa nyaraka za kieletroniki ili kuhakikisha taarifa muhimu za Taifa zinahifadhiwa kwa usalama, zinapatikana kwa urahisi na zinadumu kwa muda mrefu.

Hayo yamemwa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abulla katika maadhimisho ya siku ya nyaraka duniani kwa mwaka 2026 yaliyoadhimisha kitaifa katika viwanja vya Makumbusho ya Amani Mnazi mmoja.

Amesema katika kipindi hiki cha maendeleo makubwa ya teknolojia ya habari na mawasiliano usimamizi wa nyaraka unahitaji kwenda sambamba na matumizi ya mifumo ya kisasa ya kidijitali ili kurahisha upatikanaji wa taarifa na kuongeza ufanisi zaidi.

Mhe Hemed amesema kuwa ni matumaini ya Serikali kuwa taasisi zote za umma na binafsi zitaendelea kuzingatia viwango vya kitaalamu katika usimamizi wa nyaraka na kumbukumbu kwa lengo la kuongeza ufanisi wa utoaji huduma kwa wananchi na kulinda historia ya Taifa la Tanzania.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amesema kuwa Zanzibar imekuwa kitovu muhimu cha elimu, biashara, ustaarabu na utamaduni katika ukanda wa Afrika Mashariki na bahari ya hindi hivyo Serikali itahakikisha kuwa Manuskripti zinaendelea kuhifadhi maarifa muhimu yanayohusu dini, sheria, elimu, tiba , biashara, utawala na maisha ya jamii kwa ujumla.

Aidha amesema kuwa hati za kale ni ushahidi tosha wa mchango mkubwa wa Zanzibar katika maendeleo ya elimu na ustaarabu wa kiislamu sambamba na kuwa chanzo muhimu cha tafiti kwa watafiti , wanahistoria, wanafunzi na taasisi mbali mbali duniani.

Sambamba na hilo Mhe. Hemed amesema ni wajibu wa kila mmoja kuhakikisha kuwa manuskripti na nyaraka adhimu zinalindwa, zinatunzwa na zinaendelezwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho na kuahidi kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi mbali mbali za ndani na nje ya nchi katika kuhifadhi na kuendeleza urithi huu muhimu kwa Taifa.

Hata hivyo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ametoa wito kwa wananchi kuthamini utamaduni wa kutunza kumbukumbu na nyaraka muhimu katika maisha yao binafsi, taasisi na jamii kwa ujumla kwani Taifa lenye utamaduni wa kuhifadhi kumbukumbu zake hujenga msingi imara wa maendeleo, uwajibikaji na utambulisho wa vizazi vyake.

Nae waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Ikulu Mhe. Dkt. SAADA MKUYA SALUM amesema uwepo wa taasisi ya Nyaraka huisaidia jamii kujua umuhimu wa nyaraka na kumbukumbu katika kuhifadhi historia, kulinda haki za wananchi, kuimarisha uwazi na uwajibikaji pamoja na kuchangia maendeleo endelevu katika jamii.

Amesema nyaraka ni msingi wa kumbukumbu za Taifa zinazohifadhi ushahidi wa shughuli za Serikali na jamii pamoja na kulinda haki za wananchi, kuimarisha utawala bora na kutoa rejea muhimu kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

Aidha Dkt. Saada amefahamisha kuwa katika kuadhimisha siku ya nyaraka duniani taasisi ya nyaraka na kumbukumbu Zanzibar imeandaa na kutekeleza shughili mbali mbali ikiwewmo jukwaa la nyaraka, ziara za kijamii, maonesho ya nyaraka za kihistoria sambamba na maonesho maalumu ya maandiko ya kiislamu na hati za kiarabu.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Nyaraka na kumbukumbu Zanzibar ndugu Khatibu Suleiman Khatibu amesema taasisi hio imejipanga kutoa elimu juu ya matumizi mazuri ya nyaraka na kumbukumbu kwa maslahi ya vizazi vya sasa na baadae.

Ndugu Khatibu ametumia nafasi hio kuitaka jamii kuitumia taasisi ya nyaraka katika utunzaji wa nyaraka na kumbukumbu pamoja na kupata elimu juu ya utunzaji wa nyaraka na kujiepusha na migogoro isiokuwa na tija katika jamii

Mapema Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amekagua mabanda ya maonesho ya vitu vya asili na tamaduni za kizanzibari.









Na Mwandishi Wetu

KATIKA kuelekea kusherehekea siku ya kucheza duniani (International day of play), Shirika lisilo la kiserikali la BRAC Tanzania limewataka wazazi kutenga muda wao mzuri wa kucheza na watoto ili kuwapa ujasiri na kupata uchangamshi wa kimwili na kiakili.

Hayo yamesemwa na mkufunzi wa makuzi na malezi na maendeleo ya awali ya watoto (ECD Trainer) Mbua Dule wakati wa kuadhimisha siku hiyo ya kucheza duniani kwa kutambua umuhimu wa wazazi kushiriki kwenye michezo ya watoto.

Mbua amesema, jamii ya sasa hivi ni tofauti na jamii ya zamani ambapo wazazi wengi kwa sasa hawana muda wa kukaa na mtoto zaidi anaangalia harakati zake za kimaisha na kusahau majukumu yake kama mzazi au mlezi.

Amesema, mzazi anapocheza na mtoto kunakuwa na muunganiko mzuri wa mahusiano ya mzazi na mtoto, na uoga huwa unapungua na hata ikitokea mtoto amefanyiwa ukatili wa kijinsia wa aina yoyote ile basi anakuwa na uwezo wa kuelezea kwa mzazi wake au mlezi.

“wazazi wengi wamekuwa hawana muda wa kukaa na watoto, ukipata muda wa kucheza na mtoto wako basi unakuwa unampa ujasiri wakati wote na hata anapokwua changamoto ya kufanyiwa ukatili wa kijinsia basi anaweza akakufuata na kukuelezea jambo hilo sababu tayari anakuwa ameshajenga ukaribu Zaidi wa mtoto na mzazi,” amesema Dule.

Amesema, kila mwaka tarehe Juni 11, ni Siku ya kucheza duniani na wao kama BRAC wameamua kushiriki kwa vitendo,wakianzia kwenye maeneo ya jamii na kumalizia kwa wafanyakazi sababu hata pindi wanapliwa wanarudi nyumbani wafahamu umuhimu wa kutenga muda wa kucheza na mtoto.

“tumeanza kwenye jamii katika vituo mbalimbali vya malezi na makuzi ya awali kwa watoto lakini kwa siku ya leo tumeamua kuwashirikisha wafanyakazi , tuwaoe elimu juu ya umuhimu wa kutenga muda wa kucheza na mtoto na hata wanapokuwa wanarudi majumbani wawe wakawa mabalozi wa kuwaelimisha jamii umuhimu wa kutenga muda wa kucheza na watoto wao,”amesema Dule

Dule amesema, duniani ya sasa hivi imetawaliwa na utandawazi zipo katuni zinazotoa elimu, watoto wengi wamekuwa wanatumia muda mwingi kwenye simu za wazazi wao jambo ambalo linawanyima fursa ya kupata muda wa kucheza, hivyo basi wazazi au walezi watenge japo muda wa asilimia 20 hadi 30 kwa ajili ya watoto kucheza ili kukuza uchangamfu wa mwili na akili.

Shirika la BRAC limekuwa linatoa elimu ya makuzi na malezi ya awali kwa wanafunzi katika vituo mbalimbali na wamekuwa wanatoa elimu ya malezi kwa wazazi, ulinzia na usalama kwa watoto. Na vituo hivyo vimekuwa vinatoa fursa ya mabinti zaidi ya 300 kupata fursa ya ajira.
Wafanyakazi wa Shirika la Brac Tanzania wakicheza michezo mbalimbali wakati ya maadhimisho ya siku ya kucheza duniani iliyofanyika katika Makao Makuu ya Ofisi hiyo Jijini Dar es Salaam.





-Mauzo yake yafikia kiasi cha Sh. bilioni 33.08 ikilinganishwa na Sh.bilioni 5 zilizotarajiwa


Na Mwandishi Wetu,Michuzi TV

MAUZO ya Hatifungani ya MAKAZI ya Kampuni ya First Housing Finance Limited yamepata mafanikio ya asilimia 661.1, ambapo kiasi cha Sh.bilioni 33.08 kimepatikana, ikilinganishwa na Sh.bilioni 5 zilizotarajiwa.

Hatua hiyo inaiwezesha First Housing Finance Limited kuongeza rasilimali fedha na ukwasi, ambao utatumika kutoa mikopo ya nyumba kwa lengo la kuboresha makazi ya wananchi na kuongeza uwekezaji katika Sekta ya Nyumba na Uendelezaji Makazi.

Hayo yameelezwa leo Juni 9,2026 jijini Dar es Salaam na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana(CMSA), CPA. Nicodemus Mkama wakati wa hafla ya kuoredheshwa kwa hatifungani ya MAKAZI (MAKAZI BOND) ya Kampuni ya First Housing Finance Limited katika Soko la Hisa la Dar es Salaam.

Amesema ongezeko hilo la rasilimali fedha linatarajiwa kuiwezesha First Housing Finance Limited kuongeza ufanisi zaidi wa kutoa huduma itakayofikia makundi mengi zaidi ya wananchi kwa ujumla.

“Naufahamisha umma kuwa kati ya wawekezaji waliowekeza kwenye hatifungani ya MAKAZI, asilimia 96.63 ni wawekezaji mmoja mmoja na asilimia 3.37 ni Kampuni na Taasisi.Asilimia 96.03 ni wawekezaji wa ndani na asilimia 3.97 ni wawekezaji wa kigeni.

“Vile vile, kuorodheshwa kwa hatifungani hiyo kunaongeza thamani ya uwekezaji katika Hatifungani za Kampuni na Taasisi kwa asilimia 1.63 na kufikia Sh.trilioni 2.06, kutoka Sh.trilioni 2.03.”

Ameongeza pia ushiriki mkubwa wa wawekezaji mmoja mmoja wa ndani ni hatua muhimu katika kuongeza ukwasi (liquidity) katika soko la hisa. Aidha, hiyo ni sehemu muhimu ya utekelezaji wa Mpango Jumuishi wa Huduma za Kifedha wenye lengo la kuongeza ushiriki wa wananchi kwenye sekta rasmi ya fedha.

CPA.Mkama amesema mauzo ya hatifungani hiyo ni hatua muhimu katika utekelezaji wa Mpango Mkuu wa Maendeleo wa Sekta ya Fedha 2020/21 – 2029/30 wenye lengo la kuwezesha upatikanaji wa rasilimali fedha kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli na miradi ya maendeleo katika sekta ya umma na binafsi.

Aidha, mauzo hayo yamewezesha utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ambapo fedha zilizopatikana zitatumika kuchochea shughuli za ujenzi; kuongeza fursa za ajira kwa wananchi; kuimarisha upatikanaji na umiliki wa makazi bora na nafuu; pamoja na kuongeza ushiriki wa wananchi katika sekta rasmi ya fedha, hususan masoko ya mitaji.

“Kuorodheshwa kwa hatifungani ya MAKAZI kunatoa fursa kwa wawekezaji kuuza hatifungani zao pale watakapohitaji fedha kwa ajili ya matumizi mengine, na kuwapatia fursa wawekezaji wapya kununua hatifungani hizi.

“Uorodheshwaji wa hatifungani katika Soko la Hisa unawawezesha wawekezaji kujua thamani halisi ya hatifungani zao (Price Discovery); ambapo wawekazaji hao watapata faida ya uwekezaji wao (coupon payments).”

Ameongeza pia kuorodheshwa kwa hatifungani katika soko la hisa kunaimarisha utawala bora katika uendeshaji wa kampuni; na kumuwezesha mwekezaji kuwa na anuwai na hivyo hupunguza athari za uwekezaji (Diversification).

“Hivyo, tuna kila sababu ya kuipongeza First Housing Finance Limited pamoja na taasisi na wataalamu wote walioshiriki kuwezesha mafanikio haya. Ninatambua kazi hiyo haikuwa ndogo na rahisi lakini mmeweza kufanya kazi yenu vizuri na hivyo kufanikisha hatua hii kwa weledi na kwa ufanisi mkubwa.


“Mafanikio haya ni uthibitisho wa imani ya waliyonayo wawekezaji kwa Kampuni ya First Housing Finance na masoko ya mitaji nchini. Aidha, mafanikio haya ni matokeo ya mazingira wezeshi ya kisera, kisheria na kiutendaji yanayotolewa na Serikali katika masoko ya mitaji,”amesema CPA Mkama.

Aidha amefafanua pia mojawapo ya malengo ya DIRA 2050 ni kuona kuwa Sekta ya Fedha inawezesha upatikanaji wa rasilimali fedha kwa ajili ya kukuza na kuendeleza biashara ambazo zinachangia ukuaji na ustawi wa sekta binafsi; umma na uchumi wa nchi kwa ujumla.

“Hatifungani ya MAKAZI imetoa mchango mkubwa katika utekelezaji wa malengo haya, na ni hatua madhubuti ya kuongeza fursa za uwekezaji katika masoko ya mitaji na kuleta matokeo chanya kwenye uchumi wa nchi yetu,”amesema.










Na Mwandishi wetu, TBN, Dar es salaam

Balozi wa Uganda nchini Tanzania, Balozi Kanali Mstaafu Fred Mwesigye, ametangaza kuandaa kikao maalumu kitakachowakutanisha viongozi wa Baraza la Habari Afrika Mashariki chini ya uenyekiti wa David Omwoyo, Mtendaji Mkuu wa Baraza la Habari Kenya kujadili mikakati ya kuendeleza utalii wa kiutamaduni, uchumi wa ubunifu na sekta ya michezo inayokua kwa kasi katika ukanda huu.

Hatua hiyo inafuatia kikao cha ngazi ya juu kilichofanyika jijini Dar es Salaam kilichowakutanisha Balozi Mwesigye, Katibu Mtendaji wa Baraza la Habari Tanzania, Ernest Sungura, pamoja na wawakilishi wa Umoja Conservation Trust (UCT) wakiongozwa na Bryan Toshi , ambacho kilijadili kwa kina nafasi ya vyombo vya habari katika kujenga Shirikisho la Afrika Mashariki na kuharakisha umoja wa kikanda.

Katika kikao hicho, washiriki walikubaliana kwamba tasnia ya habari katika Afrika Mashariki inapaswa kuondokana na mtazamo wa kuripoti matukio ya kitaifa kwa namna ya kujitenga, na badala yake kujenga simulizi la kikanda linaloangazia matarajio, urithi na fursa za pamoja kwa wananchi wote.

Balozi Mwesigye alibainisha kuwa mjadala huu umejengwa juu ya maono ya kudumu ya waasisi wa Afrika Mashariki, hususan Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Mzee Jomo Kenyatta, ambayo yana umuhimu mkubwa leo kuliko wakati mwingine wowote katika historia kwani katika dunia inayozidi kutawaliwa na miungano mikubwa ya kikanda, Afrika Mashariki lazima iimarishe umoja wake ili kuongeza uimara wa kiuchumi, ushawishi wa kimkakati na ustawi wa pamoja.

Kauli hiyo pia inaenda sambamba na Hotuba ya Hali ya Taifa ya mwaka 2026 ya Rais wa Uganda, Yoweri Kaguta Museveni Tibuhaburwa, ambapo alithibitisha tena dhamira thabiti ya Uganda ya kuendeleza Shirikisho la Kisiasa la Afrika Mashariki na ushirikiano mpana wa Bara la Afrika akisisitiza kuwa ushirikiano wa kiuchumi na kisiasa ndiyo jibu sahihi kwa swali la ustawi wa kiuchumi na usalama wa muda mrefu.

Naye Ernest Sungura, ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Habari Afrika Mashariki na Katibu Mkuu wa Baraza la Habari Duniani, alieleza kuwa vyombo vya habari lazima viwe daraja linalowaunganisha wananchi badala ya kuwa mipaka inayowatenganisha, na kuongeza kuwa ushirikiano wa kikanda utafanikiwa pale wananchi watakapoanza kujiona kama Waafrika Mashariki kwa kawaida sawa na wanavyojiona kupitia mataifa yao kama Tanzania, Uganda, Kenya, Rwanda, Burundi, Sudan Kusini, Kongo au Somalia.

Kikao hicho kiliangazia changamoto ya muda mrefu inayolikabili eneo hili ikiwemo uwepo wa masoko yaliyogawanyika na mitazamo finyu ya kitaifa ambayo mara nyingi huzuia ukanda huu kufikia uwezo wake kamili, huku kikisisitiza kuwa Afrika Mashariki iliyounganishwa kikamilifu ingekuwa na nguvu kubwa zaidi ya majadiliano ya kiuchumi, soko pana, mvuto kwa wawekezaji na ushawishi mkubwa wa kisiasa duniani.

Moja ya maeneo makuu ya kimkakati yaliyojadiliwa ni maandalizi ya michuano ya kihistoria ya AFCON 2027 itakayoandaliwa kwa pamoja na mataifa ya Afrika Mashariki, ambapo Balozi Mwesigye alisisitiza kuwa mashindano hayo yanapaswa kutazamwa kama mradi wa mageuzi ya kikanda badala ya tukio la michezo pekee, kwani yanatoa jukwaa la kuonesha fursa za uwekezaji, vivutio vya utalii na uwezo wa kushirikiana kama ukanda mmoja.

Akichangia mada hiyo, Bryan Toshi wa Umoja Conservation Trust alieleza kuwa mafanikio ya kweli ya AFCON 2027 yatapimwa kwa yale yatakayotokea kabla, wakati na baada ya mashindano, huku akihimiza matumizi ya simulizi zenye uratibu ili kuzalisha ajira na kuimarisha mshikamano wa watu kwa watu.

Aidha, washiriki waligusia umuhimu wa Kiswahili kama nyenzo kuu ya kuunganisha tamaduni na diplomasia ya kikanda, ambapo walijadili uwezekano wa kushirikiana na Sekretarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ili kuanzisha rasmi Wiki ya Kiswahili ya Jumuiya ya Afrika Mashariki inayopendekezwa kufanyika kila mwaka kuanzia tarehe 1 hadi 7 Julai.

Naye Ernest Sungura alikumbusha kuwa ushirikiano wa kikanda unahusu watu kwanza, na ingawa masuala ya miungano ya forodha na korido za biashara ni muhimu, ushirikiano wa kweli hufanikiwa pale watu wanapowasiliana na kuelewana kupitia maono ya pamoja yanayojengwa na vyombo vya habari.

Ujumbe mkuu uliotoka katika kikao hicho cha Dar es Salaam ulibaki kuwa wazi kwamba Shirikisho la Afrika Mashariki halitajengwa na serikali pekee, bali litajengwa kupitia mawazo, utamaduni, lugha, michezo na simulizi zinazowaunganisha wananchi, huku vyombo vya habari vikiwa injini kuu muhimu ya kuifikisha Afrika Mashariki kwenye hatima yake ya kuwa na nguvu na ustawi wa pamoja.


Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma

Serikali imeeleza kuwa inaendelea kutekeleza mkakati wa muda mrefu wa kuwawezesha vijana, wakiwemo wenye mahitaji maalum, kupitia vikundi vilivyosajiliwa ili kuongeza ushiriki wao katika shughuli za kiuchumi na kuchangia maendeleo ya taifa.

Kauli hiyo imetolewa bungeni na Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Hamis Mwinjuma kwa niaba ya

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana, alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Latifa Khamis Juwakali, aliyetaka kufahamu mipango ya Serikali katika kuwawezesha vijana wenye vikundi vilivyosajiliwa pamoja na wenye mahitaji maalum.

Waziri huyo amesema kuwa Serikali imeweka mazingira wezeshi yanayolenga kuongeza fursa za ajira, ujasiriamali na maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa vijana kupitia programu mbalimbali za uwezeshaji.

Amefafanua kuwa uwezeshaji huo unajumuisha utoaji wa mikopo yenye masharti nafuu kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Vijana, pamoja na Programu ya Uwezeshaji Vijana Kiuchumi inayotekelezwa kupitia shilingi bilioni 200 zilizotolewa kufuatia ahadi ya Rais.

Aidha, Serikali inaendelea kutoa mikopo inayotokana na asilimia 10 ya mapato ya ndani ya halmashauri, hatua inayolenga kusaidia vikundi vya vijana kuanzisha na kuendeleza shughuli za uzalishaji mali.

Katika kuimarisha ushiriki wa makundi maalum katika uchumi, Serikali pia inaendelea kutekeleza utaratibu wa kutenga asilimia 30 ya zabuni za umma kwa vijana, wanawake na watu wenye mahitaji maalum ili kuwapa fursa zaidi za kushiriki katika shughuli za biashara na utoaji wa huduma.

Sambamba na hilo, Serikali imeendelea kuunganisha vikundi vya vijana na taasisi za kifedha pamoja na kuimarisha mifumo ya uratibu na utoaji wa taarifa, hatua zinazolenga kuongeza upatikanaji wa mitaji, fursa za biashara na ajira.

Hatua hizo zinaonesha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha vijana na watu wenye mahitaji maalum wanapata fursa stahiki za kiuchumi na kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya nchi.



Top News