Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb) amewasilisha Ujumbe Maalum kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa Rais wa Jamhuri ya Djibouti Mhe. Ismaïl Omar Guelleh wa nchi hiyo.

Mheshimiwa Kombo amewasilisha ujumbe huo wakati wa sherehe za uapisho wa Mheshimiwa Rais Guelleh zilizofanyika Mei 09, 2026 jijini Djibouti.




 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amemtembelea na kumjulia hali, Katibu Mkuu Mstaafu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na aliyewahi kuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mzee Yusuph Makamba katika makazi yake Tegeta Jijini Dar es Salaam leo tarehe 10 Mei 2026.




 

MAMIA ya wananchi wamejitokeza  kuchangia damu  katika  kambi maalumu  iliyoandaliwa na Mbunge wa  Jimbo la Ukonga,  Bakari Shingo, viwanja vya Pugu Kajiungeni, wilayani Ilala, jijini Dar es Salaam, leo.

Kambi hiyo  ilianza kwa matembezi ya hisani  ya kilometa tano yaliyoanzia Mombasa  hadi viwanja vya Pugu yakiongozwa na mbunge huyo  na kushiriki, wananchi, vikundi vya jogging na makundi mbalimbali.

Akizungumza katika kambi hiyo, Mbunge Shingo, amesema dhamira ni kuchangisha damu ili kuokoa maisha ya  watu hususan wanawake wanao jifungua, waliopata ajali, wagonjwa wa kawaida na wananchi wote  wenye matatizo ya kuhitaji damu hospitalini.

 Shingo amesema  kuchangia damu ni ibada  hivyo kuwataka wananchi kuendeleza utamaduni huo bila kujali itikadi zao za kidini na kisiasa.

“Damu hii tunayo change itakwenda kuokoa wananchi wote bila kujali dini zao wala itikadi za kisiasa.  Ofisi ya Mbunge Jimbo la Ukonga tunawashukuru wananchi waliojitokeza  leo kujitoleaa damu,”amesema Shingo.

 Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, ambaye ni Katibu Tarafa ya Ilala, Kheri William, amempongeza Mbunge Shingo kwa kuandaa kambi hiyo na kuomba utaratibu  huo uendelezwe.

“Tunaomba mbunge  huu utaratibu ulioanzisha wa kuandaa matembezi na uchangiaji damu  uendelee. Angalau kila baada ya miezi sita tuandae kambi hii,”alisema Katibu  tarafa huyo.
Alisema katika matibabu damu haina mbadala kwani haitengenezwi  kwa namna yoyote  ispo kuwa kwa wananchi kujitolea damu yao na kuokoa maisha ya wahitaji.

Zoezi la utoaji damu lilisimamia na  maofisa  wa Mpango wa Taifa wa Damu Salamaa, kutoka Hospitali ya Rufani ya Amana, ambao wamempongeza Mbunge Shingo na wananchi wote walio fika kujitolea damu kwa kuzingatia umuhimu wa uchangiaji huo









 

▪️Kumuwakilisha Rais Dkt. Samia mkutano wa ushirikiano wa Afrika na Ufaransa.

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Mei 10, 2026 amewasili Nairobi, Kenya ambako anatarajia kumuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Mkutano wa Ushirikiano wa Afrika na Ufaransa (Africa Forward: Africa–France Partnership for Innovation and Growth Summit) utakaofanyika Mei 11–12, 2026.

Lengo la mkutano huo ni kuendelea kuimarisha ushirikiano kati ya Afrika na Ufaransa katika sekta mbalimbali ikiwemo biashara, teknolojia, nishati, afya, Akili Unde (AI), kilimo, uchumi wa buluu pamoja na viwanda.

Aidha, mkutano huo unalenga kukuza uwekezaji mpya kati ya Afrika na kampuni za Ufaransa, kujenga ushirikiano unaotajwa kuwa wa usawa, pamoja na kujadili mageuzi ya mfumo wa fedha na maendeleo endelevu ya Afrika.

Mkutano huo wa Wakuu wa Nchi na Serikali unawakutanisha wadau wa maendeleo, wawekezaji pamoja na sekta binafsi, na umeandaliwa kwa ushirikiano kati ya Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mheshimiwa William Samoei Ruto, na Rais wa Jamhuri ya Ufaransa, Mheshimiwa Emmanuel Macron.








MAAFISA Habari wa Serikali wametakiwa kuongeza ufanisi katika kutangaza shughuli za Serikali huku wakizingatia mabadiliko ya teknolojia.

Msisitizo huo umetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Njombe,  Anthony Mtaka wakati akifunga Kikao Kazi cha 21 cha Maafisa Habari, Mawasiliano, Itifaki, na Uhusiano Serikalini leo Mei10, 2026.

Mtaka amewaeleza maafisa hao kuendelea kuwa daraja kati ya Serikali na wananchi kwa kuwapatia taaarifa sahihi zinazolenga kubadilisha maisha ya wananchi kupitia sekta mbalimbali ikiwemo afya, elimu pamoja na fursa zilizopo katika sekta ya burudani.

"Mnapohudhuria vikao kazi hivi tafuteni pia fursa ambazo zitabadilisha maisha yenu binafsi nje ya kazi, tafuteni uwekezaji katika biashara, kilimo na sehemu nyingine ili kuwa na maisha bora zaidi baada ya kustaafu", ameseisitiza Mtaka.

Awali Kaimu Mkurugenzi Idara ya Habari -MAELEZO  aliyemwakilisha Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Kelvin Kanje akimkaribisha Mkuu wa Mkoa ameeleza kuwa, Kikao Kazi hicho kimekuwa na mafanikio kwa kuwa maafisa wamepata elimu na mafunzo mbalimbali  yanayolenga kuongeza ufanisi katika majukumu yao.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Eleuteri Mangi, amesema kikao kazi hicho kimekuwa chachu ya maafisa kujipima utendaji kazi wao na chachu ya kufanya vizuri katika taasisi zao, akisisitiza vikao hivyo kuendelea kufanyika.

Naye Afisa Habari wa Halmashauri ya Wilaya ya Monduli,  Pettu Ogilo amesema kikao kazi hicho kimekuwa na manufaa kwake kwani masuala mengi wanayoelekezwa yanamsaidia katika utekekezaji wa majukumu yake, pia amepata elimu pamoja na kubadilishana uzoefu na maafisa wenzie. 





WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Mei 10, 2026 ameondoka nchini kuelekea Nairobi, Kenya ambako anatarajia kumuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Mkutano wa Ushirikiano wa Afrika na Ufaransa (Africa Forward: Africa–France Partnership for Innovation and Growth Summit) utakaofanyika Mei 11–12, 2026.

Lengo la mkutano huo ni kuendelea kuimarisha ushirikiano kati ya Afrika na Ufaransa katika sekta mbalimbali ikiwemo biashara, teknolojia, nishati, afya, Akili Unde (AI), kilimo, uchumi wa buluu pamoja na viwanda.

Aidha, mkutano huo unalenga kukuza uwekezaji mpya kati ya Afrika na kampuni za Ufaransa, kujenga ushirikiano unaotajwa kuwa wa usawa, pamoja na kujadili mageuzi ya mfumo wa fedha na maendeleo endelevu ya Afrika.

Mkutano huo wa Wakuu wa Nchi na Serikali unawakutanisha wadau wa maendeleo, wawekezaji pamoja na sekta binafsi, na umeandaliwa kwa ushirikiano kati ya Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mheshimiwa William Samoei Ruto, na Rais wa Jamhuri ya Ufaransa, Mheshimiwa Emmanuel Macron.





Na Pamela Mollel,Arusha 

Jiji la Arusha linaendelea kushuhudia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo inayolenga kuboresha huduma za kijamii pamoja na kuimarisha miundombinu katika maeneo tofauti ya jiji hilo. 

Hatua hiyo inaelezwa kuwa sehemu ya mkakati wa kuhakikisha Arusha linaendelea kuwa moja ya majiji muhimu nchini katika sekta ya utalii na shughuli za kikanda.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini humo, Meya wa Jiji la Arusha, Maxmillian Iranqhe, amesema katika kipindi cha robo ya tatu hadi mwisho wa mwaka wa fedha 2025/2026, halmashauri imeendelea kutekeleza miradi yenye thamani ya mabilioni ya shilingi katika kata mbalimbali kwa lengo la kuleta maendeleo kwa wananchi.

Miongoni mwa miradi inayoendelea ni ujenzi wa Kituo cha Polisi katika Kata ya Moshono unaogharimu zaidi ya shilingi milioni 145. Pia kuna ujenzi wa mtaro wa Suye wenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 100, mradi unaotarajiwa kusaidia kupunguza changamoto za miundombinu ya maji ya mvua katika eneo hilo.

Katika kuboresha mazingira na usimamizi wa taka, Halmashauri ya Jiji la Arusha inaendelea na ujenzi wa vifuko viwili vya kuhifadhi taka katika Kata ya Muriet kwa gharama inayozidi shilingi milioni 64.

 Sambamba na hilo, magari mawili mapya aina ya Toyota Pick Up yenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 363 yamepokelewa ili kusaidia shughuli za utoaji wa huduma za kijamii.

Sekta ya elimu nayo imeendelea kupewa kipaumbele ambapo ujenzi wa Shule ya Sekondari Bondeni City unaendelea kwa gharama ya zaidi ya shilingi milioni 760.

Aidha, ujenzi wa Shule ya Msingi Ungalimited nao unaendelea kwa zaidi ya shilingi milioni 877 ikiwa ni jitihada za kuongeza mazingira bora ya kujifunzia kwa wanafunzi.

Meya Iranqhe amesema utekelezaji wa miradi hiyo unaonesha dhamira ya halmashauri katika kuimarisha maendeleo ya jiji pamoja na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora zinazokidhi mahitaji yao ya kila siku.

Aidha, amewataka wananchi kuendelea kushirikiana na halmashauri katika kulinda na kuthamini miradi hiyo ili iweze kuleta manufaa ya muda mrefu kwa jamii na kuchochea maendeleo endelevu ya Jiji la Arusha.



Na  Byera Deus,Kagera 

SERIKALI kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na Benki ya Maendeleo ya kilimo(TADB) imeendelea na utoaji wa mikopo isiyo na riba na yenye masharti nafuu kwa ajili ya utekelezaji  wa miradi ya ufugaji wa samaki kwenye vizimba ili kuwezesha vijana wengi kujiajili kupitia uvuvi.

Akizungumza katika  halfa ya uzinduzi wa kukabidhi mitaji ya kuwezesha utekelezaji wa miradi iliyobuniwa  na Vijana wa (Build Better Tomorrow (BBT)-Uvuvi Mkoa wa Kagera katika mwalo wa -Bilolo Kemondo  Mwakilishi wa Katibu Mkuu Wizara hiyo Emelda Adam amesema programu hiyo inalenga kupambana na changamoto ya ajira kwa vijana na kuongeza nguvu ya vijana kujitegemea 

Amesema vijana walionufaika na vizimba mkoani Kagera walipata mafunzo ya ukuzaji wa viumbe hai mwaka 2024  na wametoka mikoa mbalimbali wakiwa wameiva kwa ujuzi wa uendeaji wa vizimba hivyo ambapo wataanza kuvuna Samaki baada ya miezi 7.

Kwa upande wake Msimamizi Mkuu wa programu ya “BBT” Kanda ya Ziwa Peter Masumbuko amesema vijana 47 wa Mkoa wa Kagera wamenufaika na programu hiyo.Shilingi bilioni saba zimetengwa kwa ajili ya vijana  zaidi ya 300 wa mikoa ya kanda ya ziwa.

Ameongeza kwa Kanda ya ziwa Program ya kuwanuia vijana mpaka kujiajiri inatekezwa mikoa ya Kagera,Mwanza ,Geita na Mara na vijana hao wote wameisha hitimu mafunzo yao

Amefafanua kwa kuanzia Kila kijana anapata kuzimba kimoja japo wanawaweka katika makundi na mradi unakuwa na  Nyumba ya mlinzi Boti ya ufatiliaji na Camera ya Kuona Nini kinaendelea katika mradi huo ambao serikali itawalea vijana kwa miaka minne Hadi wajikimu

Awali Mkuu wa Wilaya Erasto Sima kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Kagera Ramadhan  Kido amesema  ametumia nafasi hiyo kumshukuru Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kwa ajili ya programu hiyo na kuwaasa vijana wanufaika wa mkopo huo kuutumia kwa malengo yaliyokusudiwa.

Amesema baada ya ufunguzi wa vizimba mvuvi yeyote atakayekamatwa katika  eneo hilo atachukuliwa kama mvuvi haramu kwani sehemu hiyo haipaswi kusogelewa badala yake inatakiwa kulindwa Kwa nguvu zote ili kuleta matokeo Chanya .

Wakati huo huo Mwenyekiti wa Halmashauri ya Bukoba Sadothi Ijunga ameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kuukumbuka mkoa wa Kagera huku akitoa rai kwa vijana kuwa na nidhamu katika matumizi ya fedha walizozipata.

Katika hatua nyingine baadhi ya wanafuika akiwemo Marius Pius amesema  mafunzo waliyopatiwa yamehusisha vijana wa aina zote na wanamshukuru Rais Dk.Samia kwa kutimiza ahadi yake kwa vijana hao.

“Tulikuwa tayari tuko mtaani baada ya mafunzo lakini leo jambo limetimia ,hivyo sisi kama vijana lazima tusimame imara na tulete matokea chanya ambayo pia yatasaidia vijana wengine  kujiajili.Tuko tayari kulinda vizimba hivi na kuzalisha kwa weledi,”amesema Pius.












Na Said Mwishehe,Michuzi TV

SERIKALI ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dk.Samia Suluhu Hassan imeendelea kujenga mahusiano mema na nchi jirani zikiwemo za Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Mahusiano hayo ya Tanzania na nchi jirani yamekuwa ya kihistoria na chini ya uongozi wa Rais Dk.Samia umeweka msingi imara wa kuendeleza ujirani huo hasa ujirani wenye tija kwa nchi hizo.

Ujirani wetu kati ya Tanzania na nchi za jumuiya hiyo umewezesha Mei 3,2026 kushuhudia ujio wa Rais wa Rwanda Paul Kagame na Mei 4 Rais wa Jamhuri ya Kenya Dk.William Ruto .Ni safari za marais wawili tofauti lakini msingi wa safari yao ni muelekeo ule ule wa kujenga uhusiano na ujirani mwema kwa nchi hizo.

Hata hivyo ujio wa Rais Kagame na Rais Rutto pia ni uthibitisho wa nafasi ya Tanzania ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki

Kwa kukumbusha tu nafasi ya Tanzania ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) ni pana na ya kimkakati, ikihusisha historia, uchumi, siasa, na usalama wa kikanda. Hapa chini kuna maelezo ya kina yanayokupa picha kamili:

Iko hivi katika historia ya jumuiya hiyo inaonesha Tanzania ni mwanachama mwanzilishi wa EAC (toleo la sasa lililoanzishwa mwaka 2000), pamoja na Kenya na Uganda. Pia ilishiriki katika Jumuiya ya zamani ya Afrika Mashariki iliyovunjika mwaka 1977.

Tanzania imekuwa nguzo ya mshikamano wa kikanda, ikisisitiza ushirikiano wa polepole lakini thabiti (“gradual integration”).Uwepo wa Tanzania umechangia katika kuweka misingi ya sera na taasisi za EAC.

Kwa upande wa kiuchumi Tanzania ina mchango mkubwa katika uchumi wa EAC hasa katika Bandari na Biashara.Katika Bandari ya Dar es Salaam ni lango muhimu kwa biashara ya nchi zisizo na bandari kama Rwanda, Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Pia Tanzania inaunganisha ukanda wa EAC na masoko ya kimataifa kupitia Miundombinu Reli, barabara, na miradi ya nishati husaidia kuunganisha nchi wanachama.

Mfano ni miradi ya reli ya kisasa (SGR) inayolenga kuboresha usafirishaji.Miradi mingine ni Soko la Pamoja ambapo Tanzania ni sehemu ya Soko la Pamoja la EAC (Common Market) – kuruhusu uhuru wa watu, ajira, huduma na mitaji.

Mara nyingi Tanzania imekuwa makini zaidi katika kufungua soko lake kikamilifu ikilinganishwa na baadhi ya wanachama.

Kwa upande wa nafasi ya kisiasa na kidiplomasia Tanzania ina mchango mkubwa katika diplomasia ya kikanda na inajulikana kwa sera ya kutafuta maelewano na amani.Jambo kubwa na la kufurahisha zaidi Tanzania mara nyingi husimama kama mpatanishi muhimu.


Hivyo kwa ujumla, Tanzania ni mhimili wa utulivu, uchumi, na sera za tahadhari ndani ya EAC. Inachangia kwa kiasi kikubwa katika maendeleo ya jumuiya, huku ikihakikisha maslahi yake ya kitaifa hayapotei katika mchakato wa ujumuishaji wa kikanda.

Nimeeleza kwa kifupi kuhusu nafasi ya Tanzania katika jumuiya hiyo na ujio wa Rais Kagame na Rais Dk.Ruto inaendelea kuthibitisha nafasi na mchango wake kwa nchi hizo.

Hata moja ya mambo ya kuvutia kwa Rais Dk.Samia Suluhu Hassan ni kuona anaendelea kuwa daraja la mahuasiano mema kati yake na nchi jirani. Ile falsafa yake ya 4R imepenya hata katika nchi zinazoizunguka Tanzania.Hizi R4 za Mama zimepenya na kuwa nguzo ya diplomasia, amani na umoja wa Afrika Mashariki

Ikumbukwe katika kipindi cha hivi karibuni, ukanda wa Afrika Mashariki umeshuhudia mijadala mbalimbali ya kisiasa na kijamii iliyovuka mipaka ya nchi moja kwenda nyingine. 

Katika mazingira hayo, falsafa ya “R4 za Mama” imeendelea kujidhihirisha kama dira muhimu ya diplomasia, utulivu na ujenzi wa mahusiano yenye tija kwa taifa na ukanda mzima.

Kwa mtazamo wa wengi, R4 zimeonyesha msimamo wa kulinda heshima, mamlaka na uhuru wa Tanzania bila kuingia katika mvutano usio wa lazima sio tu nchini bali na kwa nchi nyingine za jumuiya ya Afrika Mashariki.

Hii ni kwa sababu taifa lolote huru lina haki ya kuendesha masuala yake ya ndani kwa mujibu wa sheria, taratibu na utashi wa wananchi wake. 

Kauli au matendo yanayoonekana kuingilia uhuru wa nchi nyingine mara nyingi huweza kuathiri mshikamano wa kikanda na kuzua taharuki zisizo za lazima.Ndio maana Rais Dk.Samia anaamini katika maridhiano zaidi .

Hata hivyo, nguvu kubwa ya R4 haipo tu katika kujibu changamoto za kisiasa, bali katika uwezo wake wa kujenga madaraja ya ushirikiano na ujirani mwema. 

Tanzania imeendelea kuonesha diplomasia ya kisasa siyo ya migogoro na majibizano, bali ni ya hekima, mazungumzo na mshikamano wa kikanda. Huo ndio msingi unaoifanya Afrika Mashariki kuendelea kuwa eneo lenye matumaini makubwa ya maendeleo ya pamoja.

Ukanda wa Afrika Mashariki una historia, tamaduni na udugu unaowaunganisha wananchi wake. Mataifa haya yanategemeana katika biashara, uwekezaji, usafirishaji, utalii na hata masuala ya usalama. 

Kwa sababu hiyo, kauli za uchochezi au matusi hazina nafasi katika kujenga mustakabali wa pamoja. Kinachohitajika ni kuheshimiana, kusikilizana na kushirikiana kwa maslahi ya wananchi wa ukanda huu.

Ujio wa Rais Kagame na Rais Rutto ni uthibitisho wa kwamba R4 zimeendelea kuonesha umuhimu wa kudumisha amani na usalama kama msingi wa maendeleo ya kiuchumi. 

Hakuna uchumi imara bila utulivu wa kisiasa, na hakuna ushirikiano wa kweli bila kuheshimu mipaka na mamlaka ya kila taifa. Tanzania, kupitia misingi hiyo, imeendelea kuwa mfano wa nchi inayotanguliza maridhiano, diplomasia na ushirikiano wa kimataifa.

Kwa ujumla, falsafa ya R4 za Mama siyo tu kauli ya kisiasa, bali ni mwelekeo unaolenga kujenga Afrika Mashariki yenye mshikamano, heshima ya mataifa, maendeleo ya pamoja na amani ya kudumu. 

Katika dunia ya leo yenye changamoto nyingi za kisiasa na kiuchumi, diplomasia ya hekima ndiyo silaha muhimu zaidi kuliko mabishano ya mitandaoni au siasa za mgawanyiko.

Wakiwa nchini Tanzania Rais Kagame na Rais Dk.Rutto kila mmoja kwa nafasi yake wamepata nafasi ya kuzungumza na mwenyeji wao Rais Dk.Samia Suluhu Hassan.

Akizungumza mazungumzo yake na Rais Kagame, Rais Dk. Samia alisema Tanzania na Rwanda  zimeendelea kujenga uhusiano wa undugu, ujirani mwema na wa kihistoria, unaoakisi  mshikamano wa muda mrefu kati ya wananchi wa pande zote.

Dk. Samia pia alisema  biashara kati ya Tanzania na Rwanda imeendelea kukua na kufikia thamani ya sh. bilioni 644 mwaka 2025 na kuanzia mwaka 1990 hadi Machi, 2026, Mamlaka ya Uwekezaji Tanzania imesajili miradi 42 ya uwekezaji kutoka Rwanda yenye thamani ya dola za Marekani milioni 325.5, iliyozalisha ajira 2,225 kwa Watanzania.

Pamoja na hatua hiyo, Rais Dk. Samia alisema nchi zote zimekubaliana kuongeza kasi ya kuondoa changamoto za kibiashara, vikiwemo vikwazo visivyo vya kikodi, kupanua biashara na uwekezaji, na kutumia kikamilifu fursa za soko la pamoja la Afrika Mashariki na Soko Huru la Biashara la Afrika.

Kama ilivyokuwa kwa Kagame, ziara ya Rais Dk.Ruto pia imebeba matumaini ya kuimarisha ushirikiano wa kindugu na kimkakati kati ya Tanzania na Kenya katika biashara, uwekezaji, miundombinu, usafirishaji na maeneo mengine ya maslahi ya pamoja.

Ukweli wa mambo ni kwamba Rais Dk. Samia Suluhu Hassan anastahili pongezi kwa kutekeleza kwa vitendo ahadi ya kujenga diplomasia ya uchumi,siasa na kijamii ambayo mwanzoni kabisa baada ya kuapishwa kushika uongozi wa nchi aliahidi kusimamia na kufanikisha hilo.

Ni wakati wa Watanzania wote kila mmoja kwa nafasi yake kutambua jitihada za Rais Dk.Samia za kuendelea kujenga mahusiano ambayo yanakwenda kufungua fursa mbambali za biashara.

Tunakumbuka wakati Rais Dk.Ruto pamoja na kuelezea masuala mbalimbali yanayohusu nchi hizo hakusita pia Kenya na Tanzania sio tu majirani bali ni ndugu wa kweli ambapo alitoa mifano kadhaa kuthibitisha anachokisema baina ya nchi hizo.

Hata hivyo nimalizie kwa kueleza hivi Tanzania chini ya uongozi mahiri wa Rais Samia iko katika mikono salama na kauli mbiu ya Kazi na Utu tunasonga mbele imekuwa faraja kwa kila mkoja wetu.


Kwa maoni 0713833822/0762451570


Na Mwandishi Wetu

KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imesema kuwa uwekezaji unaofanywa na Oryx Energies Tanzania Limited ni kielelezo cha mafanikio ya juhudi za Serikali katika kuimarisha sekta binafsi na kuongeza mchango wake katika maendeleo ya taifa.

Hayo yameelezwa leo Mei 9,2026 jijini Dar es Salaam wakati Kamati hiyo ilipotembelea sehemu maalumu ya uzalishaji wa bidhaa za Kampuni ya Oryx Energies Tanzania Limited.

Akizungumza katika ziara hiyo, Mwenyekiti wa kamati hiyo Subira Mgalu amesema kamati hiyo inatambua mchango na uwekezaji uliofanywa na Oryx Energies ambapo katika kipindi cha miaka minne imechangia pato la taita Sh.trilioni 1.2  huku pia ikiwa imetoa ajira za moja kwa moja  1000 na kwa asilimia kubwa walioajiriwa ni vijana wa kitanzania.

“Katika uwepo wa miaka 25 ya Oryx Energies nchini imetoa mchango mkubwa katika kuwezesha Watanzania kupata ajira lakini pia imekuwa na mchango mkubwa katika kuleta maendeleo na kukuza uchumi wa Taifa la Tanzania.”

“Wabunge wamepata fursa ya kuona mambo mazuri kupitia kampuni hii ikiwemo  maabara ya kisasa kwa ajili ya kupima ubora wa vilainishi lakini kwa upande wa ajenda ya matumizi ya nishati safi ya kupikia majumbani hivi sasa kumekuwepo na ongezeko kubwa la watumiaji kutoka asilimia  sita ya awali hadi kufikia asilimia 26 na ongezeko hili linakchango mkubwa wa Oryx Gas na wadau wengine.”

Aidha katika nishati safi ya kupikia amesema kamati ya nishati inampongeza Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kwani ndio kinara wa nishati safi na amekuwa akihamasisha matumizi ya nishati hiyo na sasa anatambulika katika medani za kimataifa.

Pia Mgalu amesema kamati hiyo inaendelea kusisitiza uwekezaji wenye tija na unaoleta matokeo katika taifa letu  lakini kubwa mchango wa kuinua uchumi wa nchi na watanzania kwa ujumla wake.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Oryx Energies Tanzania Limited Imani Mtafya amesema kampuni hiyo imekuwepo kwa miaka 25 sasa na uwepo wake umetoa mchango mkubwa kwa Watanzania na hasa kuhakikisha wanapata bidhaa bora hasa ya vilainishi.

Aidha amesema Oryx Energies kwa mwaka inachangia Sh.bilioni 300 ambayo ni sawa na asilimia 0.1 sambamba na kuwa na ajira asilimia 99 kwa watanzania .

Wakati huo huo Mkurugenzi wa Oryx Gas Tanzania Benoite Araman amewahakikishia wabunge wa kamati hiyo kuwa kampuni hiyo itaendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini ikiwa ni sehemu ya juhudi zao katika kuiunga mkono Serikali ambayo imelenga ifikapo mwaka 2030 asilimia 80 ya Watanzania iwe inatumia nishati safi ya kupikia.









Top News