Mbunge wa Jimbo la Katoro, Mhandisi Kija Limbu Ntemi, ametoa onyo kali kwa taasisi za kifedha zinazowadhulumu wananchi kupitia mikopo isiyo na tija, huku akiwataka wananchi kuwa makini na mikataba wanayoingia.

Agizo hilo la Mbunge limekuja baada ya kupokea malalamiko mengi kutoka kwa wananchi ambao nyumba zao zimekuwa zikipigwa mnada kwa bei ya hasara, kulinganisha na kiasi kidogo cha mkopo walichochukua.

Mhandisi Kija amebainisha kuwa hali hiyo imekuwa ikileta maumivu makali na kuwafanya wananchi wengi kubaki bila makazi huku wakikosa faida yoyote kutokana na mali zao.

Mbunge Kija ameyasema hayo leo wakati akizindua rasmi Ofisi ya Mwenyekiti wa Mtaa wa Kilimahewa, ambayo imeanza kutumika rasmi kwa ajili ya kuratibu shughuli za maendeleo na kero za wananchi wa eneo hilo.

Mhandisi Kija Amemuagiza Mtendaji wa Kata ya Ludete kuitisha mkutano wa mabalozi wa Kata za Katoro na Ludete.

Amesisitiza kuwa wananchi na mabalozi wanahitaji kupata elimu ya mahakama na taratibu za kisheria ili kutambua namna ya kutatua migogoro ya mikopo na uuzaji wa mali.

Amewatahadharisha wakopeshaji kuhakikisha taratibu zote za kiofisi na nyaraka (documents) zinazingatiwa wakati wa kukopesha na kurejesha.

"Tunaomba hili jambo lizingatiwe. Wanaokopesha wachukue tahadhari sasa; unapomkopesha mtu kwa documents, hakikisha anakulipa kwa documents. Sisi tutawashughulikia kweli ili kulinda heshima ya wananchi wetu," alisisitiza Mhandisi Kija.

Mhandisi Kija ameongeza kuwa hatanyamazia wote wanaowanyanyasa wananchi kwa kuwauzia nyumba zao bila kunufaika na chochote, na ameahidi kusimamia haki za wanyonge katika jimbo lake.











-Asisitiza amani na kuishi kindugu


WAZIRI MKUU Dkt Mwigulu Nchemba amewaomba Wabunge wa Mbulu na uongozi wa wilaya hiyo waendelee kutoa elimu kwa wananchi juu ya kuendeleza amani na kuishi kindugu.

Ametoa wito huo leo (Jumatatu, Machi 2, 2026) wakati akizungumza na wananchi waliojitokeza kwenye hospitali ya Lutheran ya Haydom, wilayani Mbulu, mkoani Manyara mara baada ya kukagua ujenzi wa jengo la afya ya mama na mtoto.

“Nimepata taarifa ya kuwepo kwa mizozo kule Yaeda Chini. Waheshimiwa Wabunge wa majimbo haya mawili na viongozi wa Halmashauri kaeni na wananchi muwaelimishe kuwa ardhi haiongezeki. Kaeni na wananchi muwaeleze kuwa suluhisho ni kupanga matumizi bora ya ardhi.”

“Endeleeni kuwaelimisha wananchi kuwa hata wakipigana ardhi haiongezeki. Hata mkiwaondoa kabila fulani, bado ardhi haiongezeki kwa sababu watu wanaendelea kuzaa.”

Akizungumzia kuhusu ujenzi wa jengo hilo, Waziri Mkuu amesifu kazi nzuri iliyofanywa na akamshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha kwa ajili ya hospitali zinazoendeshwa na taasisi za dini ili kuboresha utoaji huduma kwenye hospitali hizo.

“Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan alielekeza taasisi zinazotoa huduma kwa jamii (charitable organisations) zipewe nafuu ya kikodi. Hii ni kwa sababu hizi taasisi hazifanyi biashara na serikali inatambua mchango mkubwa unaofanywa na hizo taasisi,” amesema.

Akitoa maelezo kuhusu fedha zinazotolewa na serikali kwenye hospitali hiyo, Naibu Waziri – OWM-TAMISEMI (Elimu), Reuben Kwagilwa alisema kumekuwa na ushirikiano wa mrefua ambapo kila mwezi, Serikali imekuwa ikilipa sh. milioni 188 kwa ajili ya watumishi 128 wa hospitali hiyo.

“Serikali pia imekuwa ikitoa ruzuku ya sh. milioni 545 kila mwaka ambazo hupitia MSD kwa ajili ya ununuzi wa dawa na vifaa tiba. Vilevile, imekuwa ikitoa sh. milioni 57 kila mwaka kwa ajili ya uendeshaji wa hospitali,” amesema.

Mapema, Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania, Dayosisi ya Mbulu, Askofu John Nade alimweleza Waziri Mkuu kwamba wanashukuru kwa ushirikiano uliopo baina ya Serikali na kanisa kwenye utoaji wa huduma za jamii.

Alisema mbali na hospitali, wana Taasisi ya Afya ya Haydom ambayo inatoa mafunzo kwenye kozi tano ambazo ni Radiolojia, Famasia, Afisa Tabibu, Maabara na Uuguzi.

Akitoa taarifa ya ujenzi wa mradi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Haydom, Dkt. Paschal Mdoe alisema ujenzi wa jengo hilo umegharimu sh. bilioni 6.3 ambazo zimetokana na vyanzo vya ndani na marafiki wa Haydom Norway.

Alisema hospitali hiyo ya Kanisa imekuwa mdau mkubwa na wa muda mrefu katika sekta ya afya, ikitoa huduma za rufaa na kibingwa kwa wananchi wa Mkoa wa Manyara na mikoa jirani, pamoja na kushirikiana na Serikali katika kuboresha huduma za afya ya jamii.


TUME ya Uchunguzi wa Matukio ya Uvunjifu wa Amani yaliyojitokeza wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, leo Machi 2, 2026 imekutana na Mtaalamu wa Uchunguzi wa Kisayansi na Usalama wa Mtandao, Yusuph Kileo.

Mkutano huo wa Tume na Mchunguzi huyo umefanyika katika ukumbi wa Tanganyika uliopo jengo la Benki Kuu ya Tanzania (BoT) mkoani hapa, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Tume kukusanya taarifa, maoni na ushauri kutoka kwa watu mbalimbali wakiwemo wataalamu, watu wa kawaida, viongozi wa sasa na wastaafu.

Katika mkutano huo hoja zilizojadiliwa zilihusu maeneo ya tathmini ya athari za matukio hayo ndani ya nchi na kimataifa na ushauri wa hatua za kijamii na kisheria zinazochukuliwa ili kuimarisha amani, mshikamano wa kitaifa.

Hivi karibuni Mamlaka ya Uteuzi imeiongezea Tume muda wa siku arobaini na mbili (42) kuanzia tarehe 20 Februari, 2026 ili Tume iweze kukamilisha uchunguzi wa matukio ya uvunjifu wa amani ya wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa tarehe 29 Oktoba, 2025 na kuitaka ikamilishe kazi na kuwasilisha Taarifa yake kabla au ifikapo tarehe 3 Aprili, 2026. 

Tume inaendelea na mahojiano na waathirika wa Matukio hayo kwa ajili ya hatua zaidi kama Taifa ili Matukio kama hayo yasijirudie tena.








Msanii kutoka Zanzibar Bi Fatma Issa aliimba tahadhari na adui kiumbe, daima asikusibu na Mungu akuepushie.

Nyumbu wakiwa wanazaliwa katika eneo la Ndutu huomba sana Mungu awaepushie adui kiumbe kama Fisi, Simba, chui na mbweha ambao nao msimu huo huhamia katika eneo la Ndutu hifadhi ya Ngorongoro ili kuwavizia Nyumbu na watoto wao.

Hata hivyo kwa kuwa  Mungu ni wa wote, huwaepusha nyumbu na adui hao kwa kuwa katika  safari ya nyumbu, kuanzia wanapozaliwa Ndutu na kuanza mzunguko wa kuhama kila mwaka kuelekea  Kenya, hukabiliana na changamoto nyingi za kuliwa na wanyama wala nyama lakini wengi husalimika.

Kila nyumbu mzima (adult) ni ushahidi wa ustahimilivu mkubwa kwamba alinusurika hatari wakati wa kuzaliwa, akapita salama katika mito yenye mamba na wanyama wanaokula Nyama (Predators) katika maisha ya kila siku. Kuishi hadi utu uzima kwa nyumbu ni matokeo ya ushindi dhidi ya vikwazo vingi vya asili vilivyojaa taabu, chuki, hila na madhila.









Na Oscar Assenga,Tanga

KIKUNDI cha Amani nchini kimefanya mkutano maalumu leo katika Jiji la Tanga  uliolenga kuhamasisha uzalendo, kuelezea mafanikio ya Serikali na kupongeza utekelezaji wa ahadi za siku 100 za Rais tangu alipochaguliwa 2025.

Akizungumza wakati wa mkutano huo Maalumu Mwenyekiti wa Kikundi hicho nchini Hassan Kubebelwa alitoa wito kwa watanzania hususani vijana wametakiwa kuwa wazalendo kwa nchi na kuacha kukubali kushawishiwa na watu wanaoshinda kwenye majukwaa ya mitandao ya kijamii kueleza mabaya pekee na kuficha mazuri mengi yanayofanywa na Serikali

Katika kulitilia mkazo jambo hilo aliiomba Serikali kupitia Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) na Jeshi la Polisi, kuongeza kasi ya kuwafuatilia na kuwachukulia hatua kali watu wanaojiita wanaharakati wa mitandaoni wanaotumia majukwaa hayo kupotosha ukweli na kuichafua Serikali

"Lengo la kuja Tanga ni kuwahamasisha wanakikundi wenzetu wasimame kidete kuelezea maendeleo ya miundombinu mkoani hapa na nchi nzima. Tuache kusikiliza upotoshaji wa mitandaoni; Serikali imaleta fedha za mikopo ya asilimia 10 kwenye halmashauri, watu wakope na kujiendeleza badala ya kulalamika," alisisitiza Kubebelwa.

Awali akisoma riskala ya kikundi hicho, Mjumbe wa Kikundi hicho, Rehema Manyama alieleza katika kipindi cha siku 100, Rais ameonyesha dira kwa kufanikisha utoaji wa Bima ya Afya kwa wote, kuzalisha ajira kwa vijana ikiwemo kutoa mikopo.

Aidha alitoa ushauri wake kwa ngazi za mikoa ziendelee kutoa elimu ya uzalendo na kuimarisha elimu ya amali ili vijana wajiajiri na kuingiza kipato

 

Naye Mjumbe Zuberi Gogo, alibainisha kuwa ingawa hitilafu ndogo ndogo haziwezi kukosekana, changamoto kubwa inatokana na baadhi ya watendaji wanaopindisha taratibu na kuigombanisha Serikali na wananchi. Alitoa wito kwa wananchi kuelewa taratibu za kiserikali ili wasipotezwe na upotoshaji.

Akizungumzia suala la mikopo, Mjumbe Zainabu Salim Ugata, alifafanua kuwa mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri haina upendeleo, bali inatolewa kwa vikundi vilivyofuata taratibu zote zilizowekwa. Alisema kikundi hicho kitaendelea kuzunguka mikoa yote nchini kutoa elimu kwa umma ili kuongeza uelewa wa mambo ya Serikali.





Washiriki wa mkutano huo waliazimia kuwa ni wajibu wa kila mzalendo kuilinda taswira ya nchi na kuhakikisha kuwa fursa za kiuchumi zinazotolewa na Rais zinawafikia walengwa bila vikwazo.



WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Machi 2, 2026 amekagua Jengo la Mama na Mtoto katika Hospitali ya Kilutheri ya Haydom iliyopo Wilaya ya Mbulu, Mkoa wa Manyara, ambalo ujenzi wake umegharimu shilingi bilioni 6.3.

Mradi huo unalenga kuboresha mazingira ya utoaji wa huduma za mama na mtoto kwa kuzingatia viwango vya kisasa vya tiba na usalama wa wagonjwa na hatimaye

kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi na kupunguza msongamano wa wagonjwa wanaohitaji kupatiwa huduma hiyo.

Hospitali hiyo ya Kanisa imeendelea kuwa mdau muhimu wa Serikali katika kuboresha huduma za afya ya jamii, ikiwemo utoaji wa huduma za rufaa na kibingwa kwa wananchi wa Mkoa wa Manyara na mikoa jirani.

Akizungumza baada ya ukaguzi huo, Dkt. Mwigulu amesema kuwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anatambua kazi kubwa inayofanywa na madhehebu ya dini ikiwemo Kanisa la Kilutheri katika kuchangia ustawi wa jamii.

“Serikali iliona umuhimu wa taasisi zinazofanya kazi hii zipate misamaha ya kodi kwasababu zinashiriki kuimarisha huduma za kijamii, pia Mheshimiwa Rais Dkt. Samia anatambua kazi kubwa inayofanywa na watumishi katika sekta ya afya ikiwemo wa hapa Haydom kwa kuwa mnafanya kazi kubwa ya kuokoa uhai wa watanzania.”











Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Rais wa Jamhuri ya Ghana Mhe. John Dramani Mahama mara baada ya kuwasili katika Ikulu Ndogo ya Arusha tarehe 02 Machi, 2025. Rais wa Ghana Mhe. Mahama amewasili Mkoani Arusha kwa ajili ya Ziara ya Kikazi, ambapo anatarajiwa kuwa mgeni Rasmi katika Ufunguzi wa Mwaka mpya wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu, na Sherehe za kumbukizi ya miaka 20 tangu kuanzishwa kwa Mahakama hiyo mwaka 2006.






Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Ghana Mhe. John Dramani Mahama, katika Ikulu Ndogo ya Arusha tarehe 02 Machi, 2025. Rais wa Ghana Mhe. Mahama amewasili Mkoani Arusha kwa ajili ya Ziara ya Kikazi, ambapo anatarajiwa kuwa mgeni Rasmi katika Ufunguzi wa Mwaka mpya wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu, na Sherehe za kumbukizi ya miaka 20 tangu kuanzishwa kwa Mahakama hiyo mwaka 2006.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na Rais wa Jamhuri ya Ghana Mhe. John Dramani Mahama mara baada ya mazungumzo yao katika Ikulu Ndogo ya Arusha, tarehe 02 Machi, 2025.



NA EMMANUEL MBATILO, MICHUZI TV

Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limeendelea kuhamasisha wafanyabiashara wanawake kuthibitisha ubora wa bidhaa zao ili kukidhi matakwa ya sheria za viwango, wakati wa Maonesho ya Miaka 20 ya Tanzania Women Chamber of Commerce (TWCC) yaliyofanyika katika Viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika maonesho hayo, Meneja wa TBS Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Noor Meghji, amesema ushiriki wa shirika hilo unalenga kutoa elimu kwa wafanyabiashara wanawake, hususan wajasiriamali wadogo, ambao bado hawajathibitisha ubora wa bidhaa zao.

Amesema TBS ni mdau muhimu wa wafanyabiashara na ipo tayari kuwawezesha kufikia viwango vinavyotakiwa kisheria ili kuhakikisha bidhaa wanazozalisha zinakuwa na ubora unaokubalika sokoni.

“Tupo hapa kuhamasisha wafanyabiashara hawa waweze kukidhi vigezo vya ubora wa bidhaa zao. Tunatambua kuwa wengi wao ni wajasiriamali wadogo na wanahitaji msaada wa kitaalamu ili kufikia viwango,” amesema Meghji.

Alifafanua kuwa TBS ina programu maalumu ya kuwawezesha wafanyabiashara wanawake, hasa waliopo katika sekta ya viwanda, kwa kuwasaidia kufikia vigezo vya uthibitishaji wa ubora bila gharama.

“Tunafahamu kuna wazalishaji wengi wadogo wanawake hawana uwezo wa kumudu gharama za kuthibitisha ubora wa bidhaa zao. Kwa hiyo, tuna programu ya kuthibitisha ubora bure kwa gharama za Serikali,” ameeleza.

Kwa mujibu wa Meghji, sharti la msingi kwa mjasiriamali ni kuwa na barua ya utambulisho kutoka Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO), kisha kuwasilisha maombi TBS ambapo mchakato wa uthibitishaji huanza mara moja.

Amesisitiza kuwa hakuna sababu kwa mfanyabiashara yeyote, akiwemo mwanamke, kushindwa kukidhi viwango, akibainisha kuwa hatua hiyo itasaidia kulinda afya na usalama wa watumiaji pamoja na kupanua soko la bidhaa zao.

Kwa upande wake, mfanyabiashara Lily Mwaigomole ameishukuru TBS kwa elimu waliyoitoa, akisema imefungua uelewa wake kuhusu umuhimu wa Nembo ya Ubora ya TBS katika kukuza biashara.

“Nimefurahi kuona maofisa wa TBS wakipita kwenye mabanda wakitoa elimu kuhusu umuhimu wa kukidhi matakwa ya viwango. Mimi bado sina Nembo ya Ubora, lakini nitaanza mchakato wa kuipata ili niweze kupanua soko na kuongeza imani kwa wateja,” amesema.

Maonesho hayo ya kuadhimisha miaka 20 ya TWCC yalianza Februari 26 na kuhitimishwa Machi 2 mwaka huu, yakilenga kuwaunganisha wafanyabiashara wanawake na wadau mbalimbali wa maendeleo.






Top News