.jpeg)
Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imewakutanisha wazabuni na Taasisi Nunuzi wa mikoa ya Ruvuma, Iringa na Njombe na kuwajengea uwezo kuhusu Moduli ya kupokea na kushughulikia Malalamiko na rufaa kwenye mfumo wa NeST kwa lengo la kuimarisha utendaji kazi.
Mafunzo hayo yamefanyika kwa nyakati tofauti katika miji ya Songea na Iringa yamewahusisha washiriki 380 ambao ni wazabuni, wataalamu wa ununuzi, sheria, Tehama pamoja na makundi maalum yakiwemo wanawake, vijana, wazee na watu wenye mahitaji maalum pamoja na mafundi wa ndani.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando amesema mafunzo hayo yamekuwa yakitolewa na PPAA kwa kushirikiana na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) kwa lengo la kuwajengea uwezo wazabuni na Taasisi Nunuzi ili kuwapa ufanisi zaidi wakati wa utekelezaji wa majukumu yao, hususan katika kushughulikia malalamiko na migogoro itokanayo katika michakato ya ununuzi wa Umma.
“Mafunzo haya yanalenga kuimarisha utendaji kazi wenu, kuhakikisha ufanisi, kuongeza uelewa wa matumizi ya Moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika wa Mfumo wa Ununuzi wa Umma kwa Njia ya Kielektroniki (NeST),” amesema Bw. Sando
Bw. Sando ameongeza kuwa, katika kutimiza azma ya Serikali mafunzo yamewashirikisha vijana, wanawake na makundi maalum katika ununuzi wa umma ili kuwawezesha kupata elimu kuhusu ununuzi wa Umma hususan katika michakato ya ununuzi na kuhakikisha kuwa wanaisaidia Serikali kupata thamani halisi ya fedha katika miradi ya kimkakati yenye tija kwa Taifa.
Pamoja na mambo mengine, Bw. Sando amewasihi washiriki kutumia mafunzo hayo kujifunza namna moduli ya kuwasilisha malalamiko na rufaa inavyofanya kazi katika Mfumo wa NeST kwani inatoa njia rahisi, ya haraka na yenye uwazi kwa wadau wote kushiriki katika mchakato wa ushughulikiaji wa malalamiko yanayotokana na michakato ya zabuni za umma.
“Matumizi ya moduli yameongeza ufanisi katika usimamizi wa rufaa, kupunguza muda wa kushughulikia mashauri, na kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika utoaji wa haki, kuokoa muda na kupunguza gharama zinazohusiana na usuluhishi wa migogoro ya ununuzi,” ameongeza Bw. Sando
Kwa upande wake Meneja wa Usimamizi wa Rufaa na Sheria (PPAA), Bi. Florida Mapunda amesema kuwa mafunzo hayo yamelenga kutoa elimu kwa wadau wa ununuzi wa Umma kuhusu taratibu za uwasilishaji na ushughulikiaji wa malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST.
“PPAA kwa kushirikiana na PPRA tumejenga moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko katika mfumo wa NeST ili kuwasaidia wadau wa ununuzi wa umma (Wazabuni na Taasisi za Umma) kuwasilisha malalamiko na rufaa kwa ufanisi zaidi kupitia mtandao,” amesema Bi. Mapunda.
.jpeg)
Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando akifungua mafunzo kuhusu Moduli ya kupokea na kushughulikia Malalamiko na rufaa kwenye mfumo wa NeST kwa wazabuni na Taasisi Nunuzi wa Mkoa wa Ruvuma. Kushoto ni Meneja wa Usimamizi wa Rufaa na Sheria (PPAA), Bi. Florida Mapunda na kulia ni Mkuu wa Sehemu ya Sheria PPAA, Bi. Agnes Sayi.
.jpeg)
Meneja wa Usimamizi wa Rufaa na Sheria (PPAA), Bi. Florida Mapunda akiwasilisha mada kuhusu uwasilishaji na ushughulikiaji wa malalamiko katika mfumo wa NeST kwa wazabuni na Taasisi Nunuzi walioshiriki mafunzo mkoani Ruvuma.
.jpeg)
Afisa Sheria kutoka PPAA, Bw. Venance Mkonongo akiwasilisha mada kuhusu uwasilishaji na ushughulikiaji wa malalamiko na rufaa katika ununuzi wa umma kwa wazabuni na Taasisi Nunuzi walioshiriki mafunzo mkoani Ruvuma.
Mkuu wa Sehemu ya Sheria PPAA, Bi. Agnes Sayi akiwasilisha mada kwa washiriki walioshiriki mafunzo kuhusu Moduli ya kupokea na kushughulikia Malalamiko na rufaa kwenye mfumo wa NeST kwa wazabuni na Taasisi Nunuzi wa Mikoa ya Iringa na Njombe.
.jpeg)
Mwezeshaji kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Bw. Daniel Kimaro akiwasilisha kuhusu utoaji wa tuzo, uandaaji, upekuzi, na utiaji saini wa mkataba kwa wazabuni na Taasisi Nunuzi wa Mikoa ya Iringa na Njombe.
Sehemu ya wazabuni na Taasisi Nunuzi walioshiriki mafunzo kutoka Mikoa ya Iringa na Njombe