




MichuziBlogV2
Most read Swahili blog on earth
Bonyeza play kuangalia Michuzi TV LiVE
BONYEZA PLAY KUANGALIA AZAM TV LIVE
BONYEZA KUANGALIA CHANNEL TEN LIVE





MWANZA
Wadau wa Sekta ya Milki mkoani Mwanza wamesisitizwa kufanya kazi kwa weledi kwa kuzingatia sheria, taratibu na misingi ya taaluma ya milki ili kuhakikisha sekta hiyo inaendelea kutoa huduma bora na zenye kuaminika kwa wananchi.
Msisitizo huo umetolewa leo Machi 17, 2026 mkoani Mwanza na Kamishna wa Ardhi Msaidizi wa Mkoa huo, Bw. Wilson Luge, wakati akifunga kikao kazi cha wadau wa Sekta ya Milki kilichoandaliwa na Kitengo cha Milki kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
Amesema mafunzo na semina zinazotolewa kwa wadau wa Sekta ya Milki yana mchango mkubwa katika kuongeza uelewa wa kitaalamu pamoja na kuimarisha utendaji kazi katika kutoa huduma bora kwa wananchi, hususan katika masuala yanayohusu tathmini ya mali na usimamizi wa milki.
“Tunapenda kuishukuru Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kupitia Kitengo cha Milki kwa kutoa semina na mafunzo kwa wadau wetu wa Sekta ya Milki. Mafunzo haya yatawasaidia kuongeza ujuzi na kuimarisha weledi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku,” amesema Luge.
Aidha, amewasisitiza wadau hao wa sekta ya milki kufanya kazi kwa kuzingatia maadili ya taaluma yao na kujiepusha na vitendo vinavyokiuka sheria ikiwemo kujihusisha na masuala ya utakatishaji fedha, huku akielezea umuhimu wa kufuata taratibu zote za kisheria na kitaaluma katika kutoaji huduma za tathmini ya mali.
Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kupitia Kitengo cha Milki (Real Estate) inaendesha mijadala ya pamoja na wadau kwa lengo la kupata maoni kuhusu utambuzi na usajili wa Wadau wa Sekta ya Milki ili kuboresha na kukuza sekta ya milki nchini.
Mijadala hiyo inalenga kutoa elimu, kubadilishana uzoefu na kujadili changamoto zinazoikabili sekta ya milki nchini ambapo tayari kitengo hicho kimefanya vikao vya mijadala katika mkoa wa Dar es Salaam, Arusha, Dodoma, Tanga, Mwanza na Morogoro.

Menejimenti ya Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) kwa kushirikiana na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) imebuni mfuko wa kushirikisha wadau (stakeholders) kuwezesha kusaidia matibabu ya Upandikizaji wa Viungo kwa kuanza na Upandikizaji Uloto kwa watoto wenye Selimundu(Sickle cell) na Upandikizaji Figo kwa Wananchi wenye Uhitaji.
Akiwasilisha mpango huo kwenye mkutano wa Wenyeviti wa Bodi na Wakurugenzi wa Mashirika ambayo Serikali ina hisa ndogo (Miinority Interest Forum ) ulioandaliwa na ofisi ya Msajili wa Hazina, mjini Arusha, Mkurugenzi Mtendaji wa BMH ,Prof Abel Makubi ameeleza kuwa mfuko huo unajengwa kwa Dhana ya Wadau wenye Moyo wa Huruma wa kusaidia huduma za matibabu zenye gharama kubwa kwa Wananchi wenye uhitaji katika kuunga mkono juhudi za Serikali.
Prof. Abel Makubi ameeleza kuwa mfuko huo unachangiwa na wadau kutoka mashirika ya umma chini ya uratibu ya Msajili wa Hazina, Mashirika Binafisi na mtu mmoja mmoja , na unategemewa kukusanya TZ shilingi billion 7 ndani ya miaka miwili ili kusaidia huduma hizo katika Matibabu, vifaa, kupanua miundombinu mbinu na kuendelea kujengea uwezo watalamu wa taaluma hizo.
Mfuko huo unategemewa kuzinduliwa rasmi tarehe 8 Mei 2026 katika kilele cha Maadhimisho ya Miaka 10 ya BMH , na Wadau takribani 200 wameshirikishwa katika mpango huu .
Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. John Jingu, amesema kuanzishwa kwa Mfuko wa Pamoja wa Ruzuku kwa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGOs Basket Fund - NBF) kutarahisisha upatikanaji wa rasilimali fedha na uendelevu kwa Mashirika hayo nchini.
Akizungumza Machi 18, 2026, wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kwanza cha Kamati ya Kitaifa ya Kuratibu Mchakato wa Uanzishwaji wa Mfuko huo, kilichofanyika katika ukumbi wa Four Points by Sheraton Jijini Dar es Salaam, Dkt. Jingu amesema Mfuko huo utakuwa chombo muhimu cha kuimarisha sekta ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali.
Dkt. Jingu ameeleza kuwa hatua hiyo itasaidia kupunguza changamoto za utegemezi wa ufadhili kutoka nje ya nchi, ambao wakati mwingine huambatana na masharti magumu yasiyoendana na maadili na utamaduni wa Kitanzania.
“Jukumu la Mfuko huu litakuwa ni kutafuta rasilimali fedha, kuratibu utoaji wa ruzuku na kuhakikisha Mashirika Yasiyo ya Kiserikali yanakuwa na uwezo wa kutoa huduma bora na kuchangia ustawi wa jamii na Taifa kwa ujumla,” amesema Dkt Jingu.
Aidha, amebainisha kuwa kutokana na mabadiliko ya sera za ufadhili kimataifa, ni muhimu kwa Mashirika hayo kubadilika na kujiimarisha kwa kutumia mikakati mbadala itakayohakikisha uendelevu wa shughuli zao.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Dkt. Abdulmajid Nsekela, ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB amesema mafanikio ya utekelezaji wa majukumu ya Kamati yanategemea uwajibikaji wa kila mmoja kwa nafasi yake huku akisisitiza kuwa ni muhimu Wajumbe wa Kamati kufanya kazi kwa weledi, kwa kuzingatia misingi ya uwazi na uwajibikaji ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NacoNGO), Jasper Makala, ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, amesema Mashirika mengi kwa sasa yanafanya kazi bila uhakika wa uendelevu wa miradi yao hivyo uwepo wa Kamati hiyo itasaidia kuongeza uhakika wa rasilimali fedha na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu wa Mashirika hayo.
“Mfuko huu utakuwa suluhisho muhimu kwa changamoto ya uhaba wa rasilimali fedha na utasaidia Mashirika kupanga na kutekeleza shughuli zao kwa ufanisi zaidi,” amesisitiza Makala.
Naye Msajili wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kutoka Wizara hiyo, ambaye pia ni Katibu wa Kamati hiyo, Vikness Mayao, amesema Mfuko huo utakuwa chachu ya maendeleo kwa Mashirika hayo, kwa kuwa utaongeza tija katika utekelezaji wa miradi ya kijamii.
Ameongeza kuwa kupitia Mfuko huo, Mashirika yatapata fursa ya kufanya kazi kwa ufanisi zaidi na kuchangia kwa kiwango kikubwa katika maendeleo ya jamii na Taifa kwa ujumla..jpeg)