Na Mwandishi wetu - Msumbiji

TANZANIA  inaandaa Mpango wa Kitaifa wa Hatua za Mapema za kujiandaa, kukabiliana na ukame kwa maeneo yanayokabiliwa na janga hilo kwa kushirikiana na Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP), ikiwa ni jitihada za kupunguza athari za janga hilo nchini.

Hatua hiyo inaonesha dhamira ya serikali kuachana na utaratibu wa kusubiri madhara yatokee ndipo ichukue hatua, na badala yake kuelekea katika usimamizi wa hatari unaozingatia maandalizi na tahadhari za mapema.

Hayo yameelewa na Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Dkt. Jim Yonazi, katika ziara ya kubadilishana uzoefu kati ya Tanzania na Msumbiji kuhusu hatua za mapema kabla ya majanga unaoendelea kwa siku tano kuanzia tarehe 25 hadi 29 Mei, 2026 Mjini Maputo Msumbiji.

Alisema ukame una madhara makubwa katika kilimo, mifugo, rasilimali za maji, usalama wa chakula, maisha ya wananchi, maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa ujumla.

“Kwa sasa Tanzania inaendelea kuandaa Mpango wa Kitaifa wa Hatua za Mapema dhidi ya ukame kwa msaada wa WFP, kwa kutambua kuwa bado ni moja ya majanga makubwa yanayoathiri nchi yetu,” alisema Dkt. Yonazi.

Aliongeza kuwa mpango huo utawezesha kuwepo kwa mifumo imara ya tahadhari na utekelezaji wa hatua za mapema kabla ya majanga hayajatokea.

Kuhusu ziara hiyo, Dkt. Yonazi alisema Tanzania imechagua kujifunza kutoka Msumbiji kutokana na mafanikio yake katika kuanzisha na kutekeleza mifumo ya hatua za mapema dhidi ya majanga, hususan ukame, mafuriko na vimbunga.

Alisema kupitia ushirikiano huo, Tanzania itanufaika kwa kubadilishana uzoefu na mbinu bora, kujifunza mifumo ya uratibu wa taasisi, vigezo vya kuanzisha hatua za mapema pamoja na namna ya kugharamia hatua hizo.

Aidha, alieleza kuwa uzoefu huo utasaidia kuunganisha hatua za mapema ndani ya mifumo ya hifadhi ya jamii ili kuongeza ufanisi katika kukabiliana na majanga.

“Ziara hii ni muhimu kwa Tanzania katika kujifunza kwa vitendo na kupata mafunzo kutokana na mafanikio ya Msumbiji katika utekelezaji wa hatua za mapema kabla ya maafa,” alisema.












Na. Calvin Katera - Arusha.

Taarifa ya awali ya utafiti wa muundo wa utalii endelevu (Tourism Sustainable Model) Hifadhi ya Taifa Serengeti imewasilishwa na kujadiliwa leo Mei 25, 2026 kwa wadau zaidi ya 81 wa utalii, wawekezaji na Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) katika semina iliyofanyika ndani ya hoteli ya Mount Meru, jijini Arusha.

Tafiti hiyo iliyofanywa na wataalamu mbalimbali katika nyanja za utalii, uhifadhi na usimamizi wa fedha kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Chuo cha usimamizi wa wanyamapori (MWEKA) ililenga kuibua namna bora ya utalii wenye faida za kiuchumi bila kuathiri mazingira na ikolojia ya wanyamapori.

Akifungua Semina hiyo kwa niaba ya Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini TANAPA, Dkt. Robert Fyumagwa alieleza kuwa Dira ya Taifa ya 2050 imelenga kuhakikisha uhifadhi na matumizi endelevu ya rasilimali za asili ni kwaajili ya manufaa ya watu wote hapa nchini huku akibainisha kuwa semina hii isiishie kuthibitisha matokeo ya tafiti badala yake itoe suluhisho la vitendo.

“Tanzania imejidhatiti kupitia Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 kuhakikisha uhifadhi na matumizi endelevu ya rasilimali za asili zinawanufaisha kizazi cha sasa na vijavyo. Kazi tunayoijadili leo inaendana na azma hiyo ya Taifa.” alisema Fyumagwa.

Akiwasilisha ripoti hiyo mmoja wa timu ya washauri wataalamu Dkt. James Wakibara alieleza kuwa tafiti inaonyesha kuwa Hifadhi ya Taifa Serengeti inapokea zaidi ya watalii laki tatu kwa mwaka na bado wanaongezeka. Na moja ya sababu zinazoibua changamoto ni pamoja na baadhi ya wadau kutosimamia taratibu zilizowekwa na hifadhi (GMP - General Management Plan) katika kuwakarimu wageni pale wanapowapokea.

Naye, Mtaalamu Mshauri wa Mazingira Dkt. Flora Tibarazwa alieleza kuwa kutokana na ripoti iliyowasilishwa, TANAPA inauwezo wa kuandaa mikakati itakayowaongoza wawekezaji na wadau wa utalii kwa kuwapatia mikataba yenye miongozo itakayosimamia taratibu na sheria za uendeshaji wa biashara zao ili kuepuka uharibifu wa mazingira.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha watoa huduma za utalii nchini (TATO) na Mmiliki wa Kampuni ya Tanganyika Wilderness Camps (TWC) Willy Chambilo alieleza kuwa msongamano wa wageni hifadhini unaweza kuthibitiwa ikiwa siku za kuwakarimu wageni zitarejewa na kufanyiwa maboresho kulingana na mapendekezo ya wadau hao.

Akimwakilisha Kamishna wa Uhifadhi TANAPA, Naibu Kamishna wa Uhifadhi na Maendeleo ya Biashara Masana Mwishawa alieleza kuwa ushirikiano uliooneshwa na watafiti, wadau, wawekezaji na taasisi za uhifadhi nje na ndani ya nchi kupitia ripoti iliyowasilishwa itachangia maboresho ya mapendekezo yaliyoainishwa kwakuzingatia sheria na taratibu zinazosimamia uhifadhi na utalii ili kuendeleza uhifadhi endelevu katika sekta ya utalii.

Tafiti hii ilianza kufanyika Oktoba 2024 ikidhaminiwa na Serikali ya Ujerumani kupitia Benki ya Maendeleo ya KFW na Frankfurt Zoological Society na imekuwa kielelezo kikubwa cha tumaini kwa wadau na wawekezaji ndani ya Hifadhi ya Taifa Serengeti wakitegemea maboresho juu ya mapendekezo yaliyotewa na wadau hao.














NA Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini (TAKUKURU) imewafikisha Mahakamani  waliokuwa viongozi wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT) na watendaji wa Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA), wakikabiliwa na mashtaka ya kuunda genge la uhalifu, uhujumu uchumi na utakatishaji fedha kwa kujipatia zaidi ya Sh3.5 bilioni kwa njia za udanganyifu.

Hayo yamesemwa  na Wakili wa serikali mwandamizi Godviver Killian leo  tarehe 25 may 2026  baada ya watuhumiwa hao kufikishwa mahakamani na  kusomewa mashtaka yao katika Mahakama ya hakimu mkazi Jijini Dodoma  TEMESA wakikabiliwa na mashtaka 9 huku CWT  Mastaka 14.

Dodoma: Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini (TAKUKURU) imewafikisha katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Dodoma waliokuwa viongozi wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT) pamoja na watendaji wa Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA), wakituhumiwa kwa makosa ya kuunda genge la uhalifu,  uhujumu uchumi, utakatishaji fedha kwa kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu kiasi cha Sh3.5 bilioni

Kwa upande wa CWT, waliofikishwa mahakamani ni aliyekuwa Rais wa chama hicho Leah Ulaya, Makamu wa Rais Suleimani Ikomba, aliyekuwa Katibu Mkuu Maganga Japhet, pamoja na Joseph Misalaba, Nashon Kidudu, Baraka Mbonalibha, Wambura Kihengu, Angelina Wambura na Kampuni ya Pyrate and Industries Company Limited.

Washtakiwa hao wanakabiliwa na jumla ya mashtaka 14 ya uhujumu uchumi, ikiwemo kujipatia zaidi ya Sh2.2 bilioni kinyume cha sheria kati ya mwaka 2023 na 2024.

Akisoma mashtaka mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Dodoma, Zabibu Mpangule, Mwendesha Mashtaka Mwandamizi wa Serikali, Patrick Mwita amesema washtakiwa hao waliidhinisha matumizi ya fedha hizo kwa ajili ya ununuzi wa tisheti na kofia kinyume na Katiba ya CWT.

Mwita amedai kuwa washtakiwa hao pia walijipatia Sh1.3 bilioni kutoka Kampuni ya Pyrate and Industries Company Limited ili kupitisha zabuni ya ununuzi wa tisheti na kofia hizo kinyume cha taratibu za chama.

Aidha, amewataja wakurugenzi wa kampuni hiyo, Wambura Kihengu na Angelina Wambura, kuwa wanakabiliwa na shtaka la kughushi nyaraka mbalimbali ili kuonyesha kampuni hiyo ilikuwa halali, huku wakifahamu kuwa kitendo hicho ni kosa kisheria.

"Watuhumiwa wengine watatu ambao ni Selemani Ikomba, Baraka Mbonalibha na Angelina Wambura bado wanaendelea kutafutwa ili waunganishwe na wenzao kwenye kesi hii,” alisema Mwita.

Kwa upande wa TEMESA, waliofikishwa mahakamani ni Lazaro Kilahala, Mathias Rutaguza, Sambayeti Magoko, Kennedy Manene, Peter Bongole, Clavery Busunzu, Mbisho Kibuti, Renatha Juma, Vincent Lutembuka, Michael Assey, Caesar Chambo, Nassor Igangule, Deus Matiku pamoja na Kampuni ya Kentra Tanzania Limited.

Washtakiwa hao wanashtakiwa kwa makosa tisa ikiwemo kughushi nyaraka za ununuzi wa vipuri vya magari na kuisababishia Serikali hasara ya zaidi ya Sh1.3 bilioni.

Mwita amesema watuhumiwa wawili, Mathias Rutaguza na Michael Assey, bado wanatafutwa ili waunganishwe katika kesi hiyo.

Kwa upande wake, Hakimu Mkazi Mkuu Zabibu Mpangule amewaeleza washtakiwa kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi za uhujumu uchumi na utakatishaji fedha hadi ipokee kibali maalum kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka kutoka ofisi ya Mwanasheria mkuu wa serikali (DPP).






Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), kwa kushirikiana na Benki Kuu ya Tanzania (BOT), imeandaa semina ya pamoja uliyowakutanisha wataalamu wa Uhasibu, Wakaguzi wa hesabu na wadau wa sekta ya fedha kutoka ndani na nje ya nchi iliyoanza tarehe 25 hadi 27, Mei, 2026.

Akifungua rasmi semina hiyo iliofanyika jijini Arusha, Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) Emmanuel Tutuba, amewataka wataalamu wa fedha na Ukaguzi nchini kuhamasisha matumizi ya mifumo ya kidijitali katika miamala ya kifedha ili kupunguza matumizi ya fedha taslimu pamoja na vihatarishi vinavyoweza kujitokeza katika sekta ya fedha.

Tutuba amesema matumizi makubwa ya teknolojia katika huduma za kifedha yataisaidia Tanzania kudhibiti uvujaji wa fedha, kuongeza uwazi wa miamala na kuimarisha usalama wa mifumo ya kifedha nchini.

Ametoa wito huo katika semina ya pamoja ya wataalamu wa Uhasibu na Ukaguzi wa hesabu (NBAA) inayofanyika Jijini Arusha, akisisitiza umuhimu wa kusimamia masuala ya mabadiliko ya Tabianchi, mazingira, utawala bora pamoja na vihatarishi vinavyojitokeza kwenye sekta ya fedha kwa kuzingatia viwango vya kimataifa.

Aidha Tutuba amesema Tanzania imeendelea kuwa na uchumi himilivu licha ya changamoto za uchumi wa dunia, huku akibainisha kuwa usimamizi mzuri wa sekta ya fedha na utekelezaji wa mifumo endelevu vitasaidia Taifa kufikia dira ya uchumi wa trilioni moja.

Kwa Upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi amesema miongoni mwa mambo watakaojadili na kujifunza ni Pamoja na matumizi ya TEHAMA katika masuala yote ya fedha kupitia.

Mafunzo hayo yaliyoandaliwa na NBAA na Benki Kuu ya Tanzania (BoT) yanalenga kuimarisha mfumo wa fedha endelevu kwa kutumia teknolojia sambamba na kuzingatia misingi ya mazingira, kijamii na utawala bora katika sekta ya fedha nchini.
Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BOT), Emmanuel Tutuba akizungumza wakati wa kufungua semina ya pamoja iliyoandaliwa na NBAA na BOT iliyofanyika jijini Arusha
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi akizungumza wakati wa ufunguzi wa semina ya pamoja iliyoandaliwa na NBAA na BOT iliyowakutanisha wataalamu wa Uhasibu, Wakaguzi wa hesabu na wadau wa sekta ya fedha kutoka ndani na nje ya nchi.
Baadhi ya wataalamu wa Uhasibu, Ukaguzi wa hesabu na wadau wa sekta ya fedha kutoka ndani na nje ya nchi wakifuatilia ufunguzi wa Semina ya pamoja iliyoandaliwa na NBAA na BOT
Picha za pamoja


Na Janeth Raphael, Michuzi TV Bungeni – Dodoma

Mbunge wa Jimbo la Makete mkoani Njombe, Festo Sanga, amesema Tanzania imeendelea kuwa kivutio na kutazamwa kwa jicho la husuda na baadhi ya mataifa kutokana na hali ya amani, utulivu na mshikamano uliopo nchini, hali ambayo imekuwa ikichochea baadhi ya watu kufanya vitendo vinavyoweza kuleta mtafaruku na kuhatarisha usalama wa taifa.

Mbunge huyo ameyasema hayo leo bungeni jijini Dodoma wakati akichangia hoja ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mwaka wa fedha 2026/2027, ambapo amesisitiza umuhimu wa kuimarishwa kwa mifumo ya ulinzi na usalama kuanzia ngazi za chini kabisa za jamii.

Katika mchango wake, Sanga alitaka kurejeshwa kwa mfumo wa nyumba kumi, akieleza kuwa mfumo huo utasaidia kutambua watu wanaoingia na kutoka katika maeneo mbalimbali nchini na hivyo kurahisisha udhibiti wa uhalifu pamoja na matukio yanayoweza kuhatarisha usalama wa wananchi.

Amesema kuwa katika kipindi hiki ambacho teknolojia na mwingiliano wa watu umeongezeka kwa kasi, ipo haja ya kuwa na utaratibu madhubuti wa kufahamu taarifa za wakazi katika maeneo mbalimbali ili kuimarisha ulinzi shirikishi.

“Ni lazima kama nchi turejeshe mfumo wa nyumba kumi ili tuweze kufahamu nani anaingia na nani anatoka katika maeneo yetu. Tanzania ina amani kubwa, lakini kuna watu wanaotamani kuona nchi yetu ikiingia kwenye migogoro na machafuko, hivyo hatupaswi kubeza masuala ya usalama,” alisema Sanga.

Aidha, mbunge huyo aliibua hoja kuhusu usajili holela wa laini za simu, akisema tatizo hilo limekuwa chanzo kikubwa cha utapeli na wizi unaowaumiza wananchi wengi nchini.

Alisema bado kuna watu wanafanikiwa kusajili laini za simu katika mazingira yasiyo rasmi na bila kufuata taratibu stahiki, jambo ambalo limekuwa likitumiwa na wahalifu kufanya utapeli wa fedha pamoja na uhalifu mwingine wa kimtandao.

“Suala la usajili holela wa laini za simu limekuwa kubwa sana. Watu wanaibiwa fedha kila siku kupitia simu na matapeli wanatumia laini zilizosajiliwa kiholela. Hili suala lichukuliwe kwa uzito mkubwa,” amesema.

Kutokana na hali hiyo, aliitaka Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kushirikiana kwa karibu na vyombo vya usalama ili kudhibiti vitendo hivyo na kuhakikisha hakuna laini inayosajiliwa bila utambulisho sahihi wa mhusika.

Mbunge huyo pia alipongeza juhudi za serikali katika kuendelea kuboresha mifumo ya utambuzi wa vyombo vya moto na taarifa za wamiliki wa magari, akisema hatua hiyo imesaidia kwa kiwango kikubwa katika kusaidia ufuatiliaji wa wahalifu.

Hata hivyo, alisema bado kuna mapungufu katika maeneo ya nyumba za kulala wageni na mahotelini ambapo baadhi ya watu wamekuwa wakitumia majina yasiyo yao wanapofikia huduma hizo, hali inayoweza kuhatarisha usalama wa taifa.

Amesema ipo haja ya serikali kuweka mfumo wa kisasa wa uhakiki wa taarifa za wageni katika mahotel, nyumba za wageni na nyumba za kupanga, ambapo kila anayefikia huduma hizo atalazimika kutumia kitambulisho rasmi kama NIDA, pasipoti au kitambulisho cha mpiga kura ili taarifa zake ziweze kuhakikiwa moja kwa moja kwenye mfumo.

“Leo kuna watu wanaenda kwenye nyumba za wageni, wanaandika majina ambayo si yao, wanalala na kuondoka bila kufahamika. Ni lazima tuwe na mifumo ya verification kwenye mahotel na nyumba za kulala wageni ili jina la mtu lionekane sahihi kwenye mfumo,” amesema.

Sanga ameongeza kuwa hata kwa nyumba zinazopangishwa, ni muhimu kuwepo kwa mfumo wa uhakiki wa wapangaji ili kila anayepanga nyumba awe ametambulika rasmi, jambo litakalosaidia kupunguza vitendo vya kihalifu vinavyofanywa kwa kujificha katika makazi ya watu.

Kwa mujibu wa mbunge huyo, kuimarishwa kwa mifumo ya utambuzi na uhakiki wa taarifa za wananchi kutasaidia kuongeza usalama wa taifa, kupunguza uhalifu wa mtandao pamoja na kulinda amani na utulivu ambao Tanzania imeendelea kujivunia kwa miaka mingi.







Na Oscar Assenga, Tanga

ZAIDI ya asilimia 60 ya wagonjwa wanaopatiwa huduma katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete Cardiac Institute (JKCI) wanatoka katika mikoa ya Kanda ya Kaskazini, hali inayoendelea kuchochea ujenzi wa Taasisi kubwa ya Moyo katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC Hospital ili kusogeza huduma karibu na wananchi.

Akizungumza jijini Tanga, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Batilda Burian wakati wa mkutano wake na wana habari kuelezea harambee ya kuchangia ujenzi wa Taasisi Kubwa ya Moyo katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC utakaofanyika Mei 30 mwaka huu katika Ukumbi wa Hoteli ya Tanga Beach Resort Jijini Tanga

Alisema serikali pamoja na wadau wa maendeleo wameona umuhimu wa kuimarisha huduma za moyo Kanda ya Kaskazini kutokana na ongezeko kubwa la wagonjwa kutoka eneo hilo wanaohitaji matibabu ya kibingwa.

Alisema mradi huo utakaojengwa KCMC utakuwa na uwezo wa kutoa huduma za kisasa zinazolingana na zile zinazotolewa JKCI, na unatarajiwa kuhudumia wakazi wa mikoa ya Tanga, Kilimanjaro, Arusha na Manyara.

“Mkoa wa Tanga utaungana na uongozi wa KCMC kuhakikisha mradi huu unakamilika kwa mafanikio,” alisema Burian, akisisitiza kuwa juhudi hizo ni sehemu ya mkakati wa kuboresha sekta ya afya nchini chini ya Serikali ya Awamu ya Sita.

Burian aliongeza kuwa tayari zaidi ya Shilingi bilioni 22 zimepatikana kwa ajili ya ujenzi wa jengo hilo, huku Shilingi bilioni 3 zikihitajika kukamilisha ununuzi wa vifaa tiba vya kisasa.

Kwa mujibu wa taarifa za mradi, ujenzi tayari umeanza na umefikia asilimia 40 ya utekelezaji, huku gharama ya jumla ya mradi ikiwa ni takriban Shilingi bilioni 25.

Kwa upande wake, Meneja Miradi na Afisa Mipango wa KCMC, Emanuel Biyanchi alisema mradi huo utasaidia kupunguza rufaa za wagonjwa kwenda JKCI na nje ya nchi, hivyo kupunguza gharama kubwa kwa wagonjwa na familia zao.

“Karibu asilimia 70 ya wagonjwa wanaopewa rufaa JKCI hushindwa kufika kutokana na changamoto za usafiri na gharama, hivyo huduma zikisogezwa karibu zitakuwa nafuu na rahisi kufikika,” alisema.

Biyanchi aliongeza kuwa taasisi hiyo itakuwa msaada mkubwa katika kupunguza msongamano wa wagonjwa JKCI na kuimarisha huduma za kibingwa nchini.

Alitoa wito kwa wafanyabiashara, wananchi na wadau wa maendeleo kujitokeza kwa wingi kushiriki katika harambee itakayofanyika Mei 30 mwaka huu katika hotel ya Tanga Beach Resort ili kuchangia kukamilisha mradi huo muhimu wa afya.


Top News