Dodoma

Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila, amepongeza matumizi ya mfumo wa kisasa wa Supervisory Control and Data Acquisition (SCADA) unaotumiwa na Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA), akisema umeongeza uwazi na ufanisi katika usimamizi wa mafuta nchini.

Dkt. Nguvila alitoa pongezi hizo Juni 23, 2026, alipotembelea banda la PBPA katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali jijini Dodoma na kupata maelezo kuhusu namna mfumo huo unavyofanya kazi.

Alisema matumizi ya teknolojia za kisasa katika sekta ya mafuta yanaisaidia Serikali kufuatilia kwa karibu mwenendo wa mafuta yanayoingia nchini na kuhifadhiwa katika maghala mbalimbali, hivyo kudhibiti upotevu na kuongeza uwajibikaji.

“Ni jambo la kutia moyo kuona taasisi za umma zinatumia teknolojia za kisasa katika kuboresha usimamizi wa rasilimali za taifa. Mfumo huu unasaidia kuongeza uwazi na kuhakikisha mafuta yanayopokelewa yanafika katika maeneo yaliyokusudiwa,” alisema Dkt. Nguvila.

Akitoa maelezo kwa mgeni huyo, Mkaguzi wa Mafuta wa PBPA, Bw. Issa Khamis Mwitazy, alisema mfumo wa SCADA umechangia kwa kiasi kikubwa kudhibiti upotevu wa mafuta ambao kwa muda mrefu ulikuwa changamoto katika sekta hiyo.

Bw. Mwitazy alisema mfumo huo hulinganisha kiwango cha mafuta kilichopokelewa kutoka melini na kiwango kilichofika kwenye maghala, ambapo taarifa hutolewa mara moja endapo kutabainika tofauti yoyote ili hatua za haraka zichukuliwe.

Aidha, alisema mfumo huo unasoma na kufuatilia kwa wakati halisi ujazo wa mafuta kupitia mita za Serikali zilizopo katika bandari za Dar es Salaam, Tanga na Mtwara, pamoja na kusoma kiwango cha mafuta kilichopo katika maghala ya kampuni za mafuta.

Kwa mujibu wa PBPA, matumizi ya mfumo wa SCADA ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuimarisha usimamizi wa mafuta nchini na kuhakikisha sekta hiyo inaendeshwa kwa uwazi, ufanisi na tija zaidi.


NA: DK. REUBENI LUMBAGALA

Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ni chombo muhimu nchini katika kuhakikisha mipango na mikakati ya maendeleo inatimizwa kikamilifu. Hii inatokana na ukweli kuwa mipango mingi ya maendeleo kama uboreshaji wa sekta za elimu, afya, maji, masoko, viwanda, umeme, barabara, makazi, biashara, inategemea upatikanaji wa raslimalifedha ili ziwezeshe utekelezaji wake.

TRA ina wajibu wa kukusanya kodi kutoka kwa walipakodi wake kama wafanyabiashara, wawekezaji, wafanyakazi na wajasiriamali mbalimbali. Mafanikio ya ukusanyaji kodi, ndiyo msingi wa kuiwezesha serikali kutimiza mipango yake ya maendeleo kwa ustawi na maendeleo ya wananchi.

Sasa TRA imetimiza miaka 30 tangu kuanzishwa kwake. TRA imepata mafanikio makubwa sana hasa katika uongozi wa serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.

Rais Dk. Samia aliweka msingi wa serikali yake mapema kwa kuiagiza TRA iwajibike ipasavyo katika kukusanya mapato, lakini mapato hayo yasiwe ya dhuluma. Rais Dk. Samia anataka kila mwananchi mwenye sifa za kulipa kodi alipe.

Aprili 6, 2021, Rais Dk. Samia alipokuwa akiwaapisha makatibu wakuu na manaibu wao, alitoa maelekezo mahsusi kwa TRA. "Kukusanya kodi kwa mabavu havisaidii kwa muda mrefu. Nimepewa takwimu ya zile taskforce (vikosikazi vya kukusanya kodi) mlizoziunda lakini havisaidii, mnawatisha watu wanalazimika kufunga biashara."

"Tunazitaka kodi lakini kodi za dhuluma hapana. Kwa sababu hazitatufikisha mbali. Jinsi ya kurudisha wafanyabiashara, kutengeneza wigo wa kukusanya kodi, nafahamu uamuzi huu niliochukua tutayumba kwa miezi miwili, mitatu lakini baada ya muda tutarudi vizuri," amesema Rais Dk. Samia.

Msisitizo wa kuongeza mapato ulitokana na ukweli kuwa mipango mingi na mizuri aliyonayo Rais Dk. Samia kwa wananchi wake, haitaweza kufanikiwa kama TRA haitakusanya kodi kikamilifu ambayo ndiyo kichochea cha kufanikisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Awali, TRA ilikuwa na utaratibu wa kufunga biashara na shughuli mbalimbali pale ambapo mlipakodi atashindwa kulipa kodi kwa wakati.

Vilevile, katika makadirio ya kodi, baadhi ya wafanyabiashara walikuwa wakilalamikia kuwekewa makadirio makubwa tofauti na kiwango cha biashara zao. Hii iliweka uadui mkubwa kati ya TRA na walipakodi nchini.

MAGEUZI MAKUBWA YAMEONDOA UADUI KATI YA TRA NA WALIPAKODI

Kutokana na maelekezo ya Rais. Dk. Samia kwa TRA, uadui uliokuwepo awali kati ya TRA na walipakodi umeondoka. Hii inatokana na mtazamo chanya alioujenga Rais Dk. Samia kwa pande zote mbili.

Kimsingi, pande zote mbili zinategemeana. TRA anamtegemea mlipakodi kwani pindi kodi inapolipwa ndipo inawezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo ambayo inamnufaisha mlipakodi moja kwa moj.

Rais Dk. Samia akasisitiza pawepo na meza ya mazungumzo na makubaliano ya namna gani mlipakodi atalipa kodi pale ambapo atashindwa kulipa kwa wakati.

Aidha, Rais Samia akasisitiza kuwa kufunga biashara ni kummaliza kabisa mlipakodi kwani biashara yake itakapofungwa, ndipo atashindwa kabisa kulipa kodi kwani hatakuwa na shughuli ya kumuingizia kipato cha kuwezesha kulipa kodi na wala TRA haitaweza kupata kodi yake.

Kongole kwa Kamishna Mkuu wa TRA, Yusuph Mwenda, pamoja na wasaidizi wake nchi nzima wamefanyia kazi maelekezo ya Rais, na sasa tunashuhudia mafanikio ya kumalizika kwa uadui uliokuwepo awali.

Ni faraja kuona tunapoadhimisha miaka 30 ya TRA, kumejengeka uhusiano mzuri kati ya mlipakodi na mamlaka. Hakuna mabavu wala ubabe. Uhusiano mzuri uliopo umewezesha kuongezeka kwa mapato ya serikali.

Mathalani, mwezi Machi, 2026, TRA wamefanikiwa kukusanya trilioni 3.58, na kimsingi, ongezeko la makusanyo yamewezesha hata bajeti ya mwaka 2026/2027, kutegemea mapato ya ndani kwa asilimia 74.2.


Maoni : 0620 800 462


Na Janeth Raphael MichuziTv 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Prof. Riziki Shemdoe, ametoa maagizo ya kuchukuliwa hatua kwa maafisa rasilimali watu watakaobainika kusababisha ucheleweshaji wa upandishaji madaraja kwa watumishi wa umma, licha ya wahusika hao kutimiza vigezo vyote vinavyohitajika.

Prof. Shemdoe ametoa kauli hiyo leo wakati akifunga Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma jijini Dodoma, kwa niaba ya Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dkt. Moses Kusiluka.

Amesema kumekuwepo na changamoto ya baadhi ya maafisa rasilimali watu kushindwa kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi, hali inayosababisha watumishi stahiki kukosa au kucheleweshwa kupanda madaraja kupitia mifumo ya kiutumishi.

“Watumishi wanaostahili kupandishwa vyeo hawapaswi kukosa haki zao kutokana na uzembe wa kiutendaji wa mtu mmoja,” amesisitiza.

Katika hatua nyingine, Prof. Shemdoe ameeleza kuwa hata yeye binafsi aliwahi kukumbana na changamoto ya kucheleweshwa kupandishwa cheo kwa takribani mwaka mmoja kutokana na kutokukamilika kwa taratibu za kiutumishi kwa wakati.

Aidha, ameelekeza kufanyika kwa tathmini maalum kwa maafisa rasilimali watu wakuu wote waliohusika na ucheleweshaji wa upandishaji madaraja katika mwaka wa fedha 2025/2026, ili hatua stahiki zichukuliwe dhidi ya waliobainika na uzembe.

Prof. Shemdoe pia amewataka waajiri kuhakikisha wanatenga bajeti ya kushiriki Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, huku akisisitiza umuhimu wa maonesho hayo katika kuboresha utoaji huduma kwa wananchi.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora (OR-MUUUB), Bw. Juma Mkomi, amesema maadhimisho hayo ni sehemu ya utekelezaji wa azimio la Umoja wa Afrika linalolenga kuenzi Siku ya Utumishi wa Umma Barani Afrika.

Ameongeza kuwa lengo la maadhimisho hayo ni kutambua mchango wa watumishi wa umma katika maendeleo ya taifa, kuhamasisha ubunifu katika utoaji huduma, pamoja na kukusanya maoni ya wananchi kuhusu ubora wa huduma zinazotolewa na taasisi za umma.









-TASAC, ZMA Zaongeza Juhudi Kutatua Changamoto za Mabaharia

Na Mwandishi Wetu ,Kigoma

Serikali imesema itaendelea kuchukua hatua za kisera na kiutendaji ili kuboresha ustawi wa mabaharia nchini, ikiwemo kulinda haki zao za ajira, kuboresha mazingira ya kazi na kuhakikisha wanapata stahiki zao kwa wakati, kutokana na mchango wao mkubwa katika kukuza uchumi wa bluu.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mhandisi Ali Said Bakar, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, wakati wa ufunguzi wa Maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani yaliyofanyika mkoani Kigoma.

Mhandisi Bakar alisema mabaharia ni sehemu muhimu ya maendeleo ya sekta ya usafirishaji wa majini na uchumi wa taifa kwa ujumla, hivyo ni lazima changamoto zinazowakabili zipatiwe ufumbuzi wa haraka na wa kudumu.

Alisema Serikali inatambua kuwa baadhi ya mabaharia wamekuwa wakikumbana na changamoto mbalimbali ikiwemo kunyanyaswa kazini, mishahara kutolipwa kwa wakati, ujira mdogo na ukosefu wa huduma muhimu kama bima na matibabu, hali inayohitaji usimamizi madhubuti kutoka kwa mamlaka husika.

“Maadhimisho haya yanatoa fursa ya kutafakari mchango wa mabaharia katika maendeleo ya nchi na kuonyesha dhamira ya Serikali ya kushughulikia changamoto zao kupitia sera, sheria na hatua za vitendo,” alisema.

Aidha, alizitaka taasisi zinazosimamia sekta ya usafirishaji wa majini kuhakikisha zinakuwa mstari wa mbele katika kusimamia haki za mabaharia, ikiwemo upatikanaji wa bima, huduma za afya na mazingira salama ya kazi.

Kwa upande wake, Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma, Hassan Rugwa, alisema kufanyika kwa maadhimisho hayo mkoani humo ni ishara ya kutambua mchango wa Kigoma katika usafirishaji wa majini na maendeleo ya uchumi wa bluu.

Alisema maboresho makubwa yaliyofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika miundombinu ya usafiri wa majini yameongeza kwa kiasi kikubwa usafirishaji wa mizigo kupitia njia za maji.

“Maadhimisho ya Mabaharia kwa Kigoma yameaksi sekta ya usafirishaji ya zaidi ya asilimia 70 ya mizigo kusafirishwa kwa kutumia njia za maji katika Mkoa wa Kigoma  jambo ambalo limeongeza umuhimu wa mabaharia katika uchumi wa taifa,” alisema Rugwa.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Bahari Zanzibar (ZMA), Fatma Said Sandali, alisema ZMA kwa kushirikiana na Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) kuendelea kuweka mifumo bora ya uratibu na usimamizi ili kutatua changamoto zinazowakabili mabaharia.

Alisema maadhimisho hayo pia ni sehemu ya kuenzi mchango wa mabaharia waliopoteza maisha wakiwa kazini na kuonyesha mshikamano kwa familia zao.

Sandali alibainisha kuwa katika kipindi cha maadhimisho hayo, wananchi watapatiwa elimu kuhusu taaluma ya ubaharia, fursa zilizopo katika sekta ya usafirishaji wa baharini na maziwa, pamoja na umuhimu wa kuzingatia misingi ya kazi yenye utu, weledi na usalama.

Aliwataka mabaharia kuendelea kuzingatia nidhamu, uzalendo na taaluma katika kutekeleza majukumu yao, akieleza kuwa dunia ya sasa inahitaji mabaharia wenye ujuzi wa hali ya juu na weledi wa kimataifa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TASAC, Nahodha Mussa Mandia, alisema mabaharia ni nguzo muhimu ya sekta ya usafirishaji duniani na wanastahili kupewa kipaumbele katika mipango ya maendeleo.

Alisema Serikali imeendelea kufanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya usafirishaji wa majini, ikiwemo ujenzi wa Bandari ya Kisasa ya Kalema mkoani Katavi, ambayo inatarajiwa kuongeza biashara na kuchochea ukuaji wa uchumi wa bluu nchini.

Mandia alisisitiza kuwa pamoja na kutambua mchango wa mabaharia, ni muhimu kwao kuendelea kufuata sheria, kanuni na taratibu za kazi ili kuongeza tija, usalama na ushindani wa sekta hiyo.

Maadhimisho ya Siku ya Mabaharia Duniani mwaka huu yanatarajiwa kuhusisha utoaji wa elimu katika mialo ya uvuvi, shule na maeneo mbalimbali ya jamii kwa lengo la kuongeza uelewa kuhusu mchango wa mabaharia katika maendeleo ya uchumi wa Tanzania.

Katibu Mkuu wa Wizara Ujenzi na Uchukuzi  Zanzibar Mhandisi Ali Said Bakar akipokea zawadi kutoka kwa Mwenyekiti wa Bodi ya TASAC Nah.Mussa Mandia mara baada ya  kufungua  Maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani mkoani  Kigoma .
Katibu Mkuu wa Wizara Ujenzi na Uchukuzi  Zanzibar Mhandisi Ali Said Bakar akizungumza katika Ufunguzi wa  maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani mkoani  Kigoma .




Matukio mbalimbali katika picha wakati wa ufunguzi wa Maadhimisho ya 16 ya Siku Mabaharia Duniani.


Na Victor Masangu,Pwani


Mamlaka ya mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Pwani katika kipindi cha miaka kumi iliyopita kuanzia mnamo mwaka 2015 hadi mwaka 2026 imefanikiwa kufanya vizuri baada ya kukusanya kodi kiasi cha shilingi bilioni 266.

Hayo yamebainishwa na Meneja wa TRA Mkoa wa Pwani Peter Eliona wakati wa halfa ya kongamano maalumu ambalo limewajumuisha wadau mbali mbali pamoja na walipa kodi ikiwa ni katika kuelekea maadhimisho ya miaka 30 ya TRA.

Meneja huyo amebainisha kwamba fedha hizo zimekusanywa kutokana na kuwepo kwa mfumo mizuri waliyoiweka katika suala zima la ukusanyaji ikiwemo pamoja na kuwashirikisha walipa kodi.

Aidha meneja huyoo amesema kwamba lengo kubwa TRA ni kuendelea kuweka mikakati ya kuendelea kukusanya kodi ambayo imekuwa ni mkombozi katika kutekeleza miradi mbali mbali ya maendeleo.

"Leo tumekutana katika kongamano hili ambalo tumeweza kuwashirikisha sadau wetu wa maendeleo pamoja na walipa kodi ili kuweza kujadili mambo mbali mbali ya ulipaji wa kodi,"amebainisha Meneja huyo.

Naye Mwenywkiti wa Chama cha Wafanyabiashara Mkoa wa Pwani Abdallah Ndauka amesema ili kuongeza makusanyo TRA wanatakiwa kuangalia namna ya kuwasaidia wafanyabiashara wasifunge biashara zao badala yake wajikite kushauri kuwasaidia kuendelea zaidi.

Amesema kwamba wapo wafanyabiashara wanafunga biashara zao kutokana na sababu mbalimbali ili kunusuru hilo ni vema watumishi wa Mamlaka hiyo wakawa msaada wa kuzifufua ili waendelee kupata kodi.

Pia, ameiomba TRA mkoa wa Pwani kuwa sehemu ya kutoa fursa kwa wafanyabiashara hao ili kukuza biashara zao kwa kununua vifaa na samani nyingine badala ya kuagiza nje ya nchi.

Mamlaka ya Mapato (TRA)) Mkoa wa Pwani imekuwa ikishirikiana bega kwa bega na walipa kodi pamoja na kutoa mafunzo ambayo yamesaidia kuongeza kasi ya ukusanyaji wa mapato na kuvuka malengo.


Na Mwandishi Wetu, Kigoma

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), Mohamed Salum, amesema kuwa usafiri wa meli ya MV Liemba una umuhimu mkubwa kwa wananchi wanaotegemea huduma za usafiri wa majini katika ukanda wa Ziwa Tanganyika, huku akieleza kuwa meli hiyo itakuwa chachu ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Salum alitoa kauli hiyo wakati alipotembelea eneo la ujenzi wa meli ya MV Liemba mjini Kigoma katika maadhimisho ya Siku ya Mabaharia yanayoendelea mkoani humo.

Amesema kuwa wananchi wengi wa maeneo yanayozunguka Ziwa Tanganyika wanategemea usafiri wa majini kwa shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi, hivyo kukamilika kwa ujenzi wa meli hiyo kutasaidia kuboresha huduma za usafiri na usafirishaji wa bidhaa.

“Meli ya MV Liemba ni muhimu kwa wananchi wetu kwa sababu inatoa huduma zinazogusa maisha ya kila siku ya watu wengi. Kukamilika kwake kutaimarisha usafiri salama na wa uhakika katika maeneo yanayohudumiwa na meli hiyo,” amesema Salum.

Aliongeza kuwa katika mkoa wa Kigoma, MV Liemba itaendelea kuwa nyenzo muhimu ya kuchochea shughuli za biashara, kuunganisha jamii na kurahisisha upatikanaji wa huduma mbalimbali za kijamii kwa wananchi wa ukanda huo.

Salum amesema uwekezaji unaofanyika katika kuboresha meli hiyo unaonesha dhamira ya Serikali ya kuimarisha sekta ya usafiri wa majini na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora zinazochangia ukuaji wa uchumi wa bluu nchini.

Ziara hiyo ni sehemu ya shughuli za Maadhimisho ya Siku ya Mabaharia ambayo yanalenga kutambua mchango wa mabaharia na wadau wa sekta ya usafiri wa majini katika maendeleo ya taifa.



Wataalamu wa afya, watafiti, viongozi wa vijana na wadau mbalimbali wa maendeleo kutoka ndani na nje ya Afrika wamekutana jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kujadili namna ya kuimarisha huduma na sera za afya kwa vijana balehe barani Afrika.

Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa na Mtandao wa ARISE kupitia Mkurugenzi Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Afya ya Umma, Dkt. Mary Mwanyika Sando, Juni 22, 2026, inaeleza kuwa Mkutano wa 2026 wa Afya ya Vijana Balehe Kusini mwa Jangwa la Sahara (CAH-SSA) pamoja na Mikutano ya Mwaka ya Mtandao wa Utafiti, Sayansi ya Utekelezaji na Elimu Afrika (ARISE), unafanyika kuanzia Juni 22 hadi 25, 2026 Jijini Dar es Salaam.

Mkutano huo unafanyika chini ya kaulimbiu “Kuonesha Mafanikio ya Afua Endelevu za Afya ya Vijana Balehe Zinazoongozwa na Jamii”, ukiwa na lengo la kuonesha matokeo ya tafiti na kujadili mbinu bora za kuboresha afya ya vijana.

Mgeni rasmi katika mkutano huo ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Tanzania, Dkt. Seif Abdallah Shekalaghe, ambaye amezungumzia namna matokeo ya tafiti yanavyoweza kutumika kuboresha sera za afya, kuimarisha huduma kwa vijana na kuongeza ushiriki wa vijana katika ubunifu na utekelezaji wa afua zinazowahusu.

Mkutano huo umewakutanisha wadau mbalimbali wakiwemo Serikali, washirika wa maendeleo, viongozi wa vijana, watafiti, taasisi za utafiti na sekta binafsi kwa lengo la kujenga ushirikiano wa kuongeza matokeo chanya katika afya ya vijana barani Afrika.

Katika mkutano huo, vijana pia wamepewa nafasi kupitia Wawakilishi wa Bodi ya Ushauri ya Vijana Balehe na Vijana kwa ujumla (AYAB), akiwemo Mtanzania Bi. Mariam Surve na Bi. Mariam Yusuff kutoka Nigeria, ambao wanawakilisha sauti na mahitaji ya vijana katika uundaji na utekelezaji wa programu za afya.

Miongoni mwa maeneo yatakayojadiliwa ni matokeo ya miradi ya DASH na ARISE-NUTRINT inayolenga kuboresha afya ya vijana katika maeneo ya lishe, mazoezi, afya ya uzazi na afya ya akili. Miradi hiyo imefadhiliwa na Serikali ya Ujerumani pamoja na Umoja wa Ulaya.

Aidha, mkutano huo unalenga kuimarisha mipango ya Mtandao wa ARISE kwa kipindi cha mwaka 2026–2027 kwa kuweka mikakati itakayowezesha afua za afya kwa vijana kuwa endelevu kifedha na kutekelezwa kwa upana katika ngazi za jamii, kitaifa na kikanda.

Wakizungumza kuhusu umuhimu wa mkutano huo, viongozi wa ARISE wamesema jukwaa hilo ni muhimu katika kuunganisha tafiti, matokeo yake, sera na utekelezaji wa programu zinazolenga kuboresha maisha ya vijana barani Afrika.

Mtandao wa ARISE ni ushirikiano wa taasisi za Afrika na mabara mengine unaolenga kuimarisha uwezo wa utafiti wa afya ya umma na kuendeleza utekelezaji wa afua zenye msingi wa ushahidi, ukiwa na zaidi ya taasisi 22 kutoka nchi mbalimbali Kusini mwa Jangwa la Sahara.










Na Oscar Assenga, Muheza

WANANCHI 6,258 wa Kijiji cha Muungano, Wilaya ya Muheza, wamenufaika na huduma bora za afya kufuatia kukamilika kwa ujenzi wa Zahanati ya Muungano, mradi ambao umepokelewa na kuridhiwa na Mwenge wa Uhuru 2026 baada ya kukaguliwa na kupokea taarifa ya utekelezaji wake.

Akizungumza wakati wa ukaguzi wa mradi huo, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026 Wazo Mwang'onda alisema kukamilika kwa zahanati hiyo kumesaidia kusogeza huduma za matibabu karibu na wananchi na kupunguza changamoto ya kusafiri umbali mrefu kufuata huduma za afya.

Alisema Serikali tayari imepeleka vifaa tiba pamoja na watumishi wa afya watakaotoa huduma katika zahanati hiyo, hatua inayoonesha dhamira ya kuboresha upatikanaji wa huduma za afya, hususan katika maeneo ya vijijini.

“Mradi huu ni muhimu kwa wananchi wa Muungano na maeneo jirani kwa sababu unasaidia kuboresha upatikanaji wa huduma za afya na kuongeza ustawi wa jamii,” alisema.

Kiongozi huyo aliongeza kuwa mafanikio ya mradi huo yametokana na ushirikiano kati ya Serikali na wadau wa maendeleo, hususan Taasisi ya Islamic Help, iliyochangia ujenzi wa zahanati hiyo, huku Serikali ikigharamia vifaa tiba na watumishi wa afya.

Aliwashukuru wadau wa maendeleo kwa kuendelea kushirikiana na Serikali katika utekelezaji wa miradi ya kijamii, na kuwataka kuendeleza ushirikiano huo ili kusaidia kuboresha huduma muhimu kwa wananchi.

Aidha, aliwahimiza wananchi kuendelea kulinda amani na utulivu wa nchi, akisema kuwa mazingira hayo yanawezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuvutia wadau zaidi kushirikiana na Serikali.

Kwa upande wake, akitoa taarifa ya mradi huo, Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Muheza, Dk. Fani Mussa, alisema ujenzi wa Zahanati ya Muungano ulianza Machi 2, 2025 na kukamilika kwa gharama ya Shilingi milioni 165.94.

Alieleza kuwa kati ya fedha hizo, Shilingi milioni 141.55 zilitumika kwa ujenzi, huku Shilingi milioni 24.39 zikitumika kununua vifaa tiba.

Kwa mujibu wa Dk. Mussa, zahanati hiyo itahudumia wakazi 6,258 wa Kijiji cha Muungano, wakiwemo wanaume 3,089 na wanawake 3,169, na inatarajiwa kwa kiasi kikubwa kuboresha upatikanaji wa huduma za afya katika eneo hilo.

Baada ya ukaguzi huo, Mwenge wa Uhuru 2026 ulieleza kuridhishwa na ubora wa utekelezaji wa mradi huo, ukibainisha kuwa ni hatua muhimu katika kusogeza huduma za afya karibu na wananchi na kuunga mkono jitihada za Serikali za kuimarisha sekta ya afya nchini.



Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa akizungumza kwa  niaba ya Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati akifungua mkutano wa tatu wa Kimataifa wa Kimkakati wa kikanda wa Pen-Plus kuhusu kukabiliana na magonjwa yasiyoambukiza makali (ICPPA 2026) unaofanyika kwa siku gatu kuanzia leo Juni 23, 2026 katika ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa JNICC, jijini Dar es Salaam.


Na Karama Kenyunko,Michuzi TV
WAZIRI wa Afya, Mohamed  Mchengerwa, amesema hakuna maisha ya mwafrika yanayopaswa kupotea kwa sababu huduma za afya zilikuwa mbali, ghali au zilichelewa kupatikana.

Akizungumza katika ufunguzi wa Mkutano wa Tatu wa Kimataifa wa PEN-Plus Afrika 2026, Mchengerwa alisema ukweli unaotia wasiwasi ni kwamba vifo vingi vya mapema vinavyotokana na magonjwa yasiyoambukiza hutokea katika nchi zenye kipato cha chini na cha kati, nyingi zikiwa barani Afrika.

“Hili si suala la kitabibu pekee; ni suala la usawa. Ni swali la kama mahali alipozaliwa mtu, anapoishi au kipato chake kinaweza kuamua kama atapata huduma bora kwa wakati,” alisema.

Alisema Tanzania imeamua kusogeza huduma karibu na wananchi kwa kuhakikisha asilimia 80 ya jamii zinafikia huduma za afya ndani ya umbali wa kilomita tano kutoka makazi yao.

Mchengerwa alisema mkakati wa PEN-Plus umeendelea kuwa moja ya ubunifu muhimu zaidi barani Afrika kwa kuwezesha huduma za magonjwa sugu na magonjwa yasiyoambukiza kutolewa katika hospitali za wilaya na vituo vya afya badala ya kutegemea hospitali za rufaa pekee.

“Huduma maalumu hazipaswi kubaki katika hospitali za rufaa zilizoko mbali wakati wagonjwa wanahitaji msaada endelevu karibu na jamii zao,” alisema.

Alibainisha kupitia ushirikiano wa serikali na wadau mbalimbali pamoja na Programu ya Samia Suluhu Outreach, huduma za PEN-Plus zinaendelea kupanuliwa nchini hususan katika maeneo ya vijijini na yaliyokuwa nyuma kimaendeleo.

Alizitaka nchi za Afrika kuongeza fedha za ndani kwa ajili ya afya, kuimarisha tafiti na ubunifu, kuboresha upatikanaji wa dawa na teknolojia za afya pamoja na kujenga mifumo imara ya afya.

“Afya ndiyo msingi wa maendeleo endelevu. Taifa linalowekeza katika afya linawekeza katika nguvu kazi yake, watoto wake, wanawake wake, wazee wake, uzalishaji wake na mustakabali wake,” alisema.



Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa akizungumza kwa  niaba ya Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati akifungua mkutano wa tatu wa Kimataifa wa Kimkakati wa kikanda wa Pen-Plus kuhusu kukabiliana na magonjwa yasiyoambukiza makali (ICPPA 2026) unaofanyika kwa siku gatu kuanzia leo Juni 23, 2026 katika ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa JNICC, jijini Dar es Salaam
Mkurugenzi wa WHO Kanda ya afrika, Profesa Mohamed Janabi akizungumza  wakati ufunguzi wa mkutano wa tatu wa Kimataifa wa Kimkakati wa kikanda wa Pen-Plus kuhusu kukabiliana na magonjwa yasiyoambukiza makali (ICPPA 2026) unaofanyika kwa siku gatu kuanzia leo Juni 23, 2026 katika ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa JNICC, jijini Dar es Salaam
Ofisa Programu wa PEN-Plus kutoka Helmsley Charitable Trust,  James Reid  akizungumza wakati ufunguzi wa mkutano wa tatu wa Kimataifa wa Kimkakati wa kikanda wa Pen-Plus kuhusu kukabiliana na magonjwa yasiyoambukiza makali (ICPPA 2026) unaofanyika kwa siku gatu kuanzia leo Juni 23, 2026 katika ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa JNICC, jijini Dar es Salaam




Na Karama Kenyunko Michuzi Tv
WAZIRI wa Afya, Mohamed Mchengerwa, amesema ongezeko la magonjwa yasiyoambukiza barani Afrika linatishia maendeleo ya kijamii na kiuchumi, akisisitiza kuwa bara hilo haliwezi kujenga uchumi imara huku likiendelea kubeba mzigo wa magonjwa ambayo hayapati matibabu kwa wakati.

Mchengerwa amesema hayo kwa niaba ya Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dk Samia Suluhu Hassan wakati wa mkutano wa tatu wa Kimataifa wa Kimkakati wa kikanda wa Pen-Plus kuhusu kukabiliana na magonjwa yasiyoambukiza makali (ICPPA 2026) leo Juni 23, 2026 jijini Dar es Salaam

Amesema magonjwa yasiyoambukiza kama kisukari, shinikizo la damu, saratani, magonjwa ya moyo na selimundu yanaongezeka kwa kasi na kuathiri uzalishaji pamoja na ustawi wa familia.

kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), magonjwa yasiyoambukiza husababisha zaidi ya vifo milioni 43 duniani kila mwaka, sawa na asilimia 74 ya vifo vyote.

Hivyo, Mchengerwa amesema Tanzania imeongeza uwekezaji katika kukabiliana na magonjwa hayo kwa kuongeza bajeti ya huduma husika kutoka asilimia saba ya matumizi ya afya mwaka 2020 hadi zaidi ya asilimia 24 mwaka 2024, sambamba na kuboresha vifaa vya uchunguzi na matibabu nchini.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa WHO Kanda ya Afrika, Profesa Mohamed Janabi, amesema magonjwa yasiyoambukiza si tishio la baadaye bali ni changamoto ya sasa inayohitaji hatua za haraka za kuimarisha kinga, uchunguzi wa mapema na huduma za afya ya msingi.

Amesema wagonjwa wengi barani Afrika bado hugundulika katika hatua za mwisho za ugonjwa, hali inayochangia kuongezeka kwa vifo na gharama kubwa za matibabu kwa familia na serikali.

Amesisitiza kuwa kuwekeza katika kinga na uchunguzi wa mapema ni hatua muhimu katika kupunguza mzigo wa magonjwa hayo.

Profesa Janabi pia aliipongeza Tanzania kwa mafanikio yake katika sekta ya afya, ikiwemo kupunguza kwa kiwango kikubwa vifo vya wajawazito, hatua aliyosema imeokoa maisha ya maelfu ya wanawake na kuziwezesha familia nyingi kuendelea kuwa pamoja.

Pia, alimpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutambuliwa kama Bingwa wa Afya ya Mama Barani Afrika, akisema mafanikio hayo yanaonyesha dhamira ya uongozi wa Tanzania katika kuboresha huduma za afya na ustawi wa wananchi.

Naye Ofisa Programu wa PEN-Plus kutoka Helmsley Charitable Trust, James Reid, amesema zaidi ya wagonjwa 170,000 katika nchi 20 za Afrika tayari wamenufaika na huduma zinazotolewa kupitia mpango huo, ambao unalenga kusogeza huduma za magonjwa sugu karibu na wananchi.

Amesema mafanikio yaliyopatikana katika nchi mbalimbali yanaonyesha umuhimu wa serikali kuendelea kuwekeza katika mifumo ya afya na kuhakikisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi wengi zaidi.

Reid ameongeza kuwa ushirikiano kati ya serikali, wadau wa maendeleo na taasisi za afya ni muhimu katika kupanua huduma za PEN-Plus na kuhakikisha watu wengi zaidi wenye magonjwa sugu wanapata matibabu kwa wakati.


Na Mwandishi Wetu, Tabora
SERIKALI imezindua rasmi Mradi wa Uhifadhi wa Bioanuai, Usimamizi Endelevu wa Ardhi na Kuongeza Usalama wa Maji katika Bonde la Ziwa Tanganyika, hatua inayolenga kuimarisha uhifadhi wa mazingira, kulinda vyanzo vya maji na kuboresha maisha ya wananchi wanaoishi katika maeneo ya bonde hilo.

Uzinduzi wa mradi huo ulifanywa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Tabora, Ally Babu, ambaye alisema mradi huo ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuhakikisha rasilimali za asili zinatumika kwa njia endelevu kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi huo, Babu alizitaka taasisi za umma, washirika wa maendeleo na wananchi kushirikiana kikamilifu katika utekelezaji wa mradi ili kufanikisha malengo yaliyowekwa.

Alisema mradi huo utachangia kuimarisha uhifadhi wa bioanuai, matumizi bora ya ardhi na usalama wa maji, huku ukiwanufaisha wananchi wanaotegemea rasilimali za Bonde la Ziwa Tanganyika kwa shughuli za kilimo, uvuvi na ufugaji.

“Ni muhimu wadau wote tushirikiane kwa karibu ili kuhakikisha mradi huu unaleta matokeo yaliyokusudiwa. Mafanikio yake yatachangia uhifadhi wa mazingira, kuimarisha usalama wa maji na kuboresha ustawi wa wananchi,” alisema Babu.

Aliongeza kuwa Serikali inatarajia kuona utekelezaji wa haraka wa shughuli za mradi huo ili manufaa yake yaanze kuonekana kwa wananchi na mazingira kwa ujumla.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Bodi ya Maji Bonde la Ziwa Tanganyika, Bona Mremi, alisema Bonde la Mto Malagarasi limepewa kipaumbele katika utekelezaji wa mradi kutokana na mchango wake mkubwa katika kuhifadhi mfumo wa ikolojia wa Ziwa Tanganyika.

Alisema bonde hilo lenye ukubwa wa takribani kilomita za mraba 67,000 na wakazi wapatao milioni sita ni chanzo muhimu cha maji yanayoingia katika Ziwa Tanganyika, hivyo uhifadhi wake ni muhimu kwa mustakabali wa ziwa hilo.

Mradi huo unatarajiwa kuwa chachu ya maendeleo endelevu kwa kuchochea uhifadhi wa mazingira, usalama wa maji na matumizi endelevu ya ardhi katika Bonde la Ziwa Tanganyika, huku ukilinda rasilimali muhimu kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

Top News