

MWENYEKITI wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) Deodatus Balile, amesema matukio ya waandishi wa habari kukamatwa, kupigwa na kubughudhiwa yamepungua kwa kiasi kikubwa ukilinganisha na hali ilivyokuwa huko nyuma.
Balile amesema hayo leo Aprili 16, 2026 wilayani Temeke mkoani Dar es Salaam katika ufunguzi wa Mkutano Mkuu Maalumu wa jukwaa hilo uliofanyika kwa lengo la kujadili mapendekezo ya marekebisho ya Katiba.
Akizungumzia hali ya vyombo vya habari nchini na mataifa mengine, Balile amesema kumetokea mambo mengi yakiwemo waandishi kupoteza maisha, vyombo vya habari kufungwa na kukabiliwa na hali ngumu ya kiuchumi.
“Mataifa mbalimbali duniani tumeshuhudia mambo mengi yakitokea katika miaka ya karibuni kwenye tasnia yetu ya habari.
“Waandishi 140 wamepoteza maisha kutokana na vita zinazoendelea kwa baadhi ya nchini, lakini tumeshuhudia katika vyombo vya wenzetu wamepata mtanzuko mkubwa na sasa hivi Sauti ya Amerika (VOA) haipo hewani na chaneli zake zote.
“Pia katika nchi za jirani kuna waaandishi wamezuiliwa kuingia katika nchi. Kwa Tanzania matukio ya waandishi wa habari kukamatwa, kupigwa imepungua kwa kiasi kikubwa ukilinganisha na zamani.
“Nimekuwa Rais wa Jukwaa la Wahariri la Afrika Mashariki kwa muda mrefu, na nchi ambazo ni wanachama wa jukwaa hilo wanakiri Tanzania iko vizuri, lakini ni wajibu wetu sasa kuzingatia misingi ya taaluma ya habari," amesema.
Akieleza zaidi Balile amesema kuna baadhi ya waandishi wa habari wamekuwa wakiogopa kuandika kabla ya kuzuiliwa kwa maana ya kujizuia kuandika kabla ya kuzuiwa, hivyo ametoa rai ya kuondoa woga huo huku akisisitiza kutekeleza majukumu yao kwa kufuata misingi ya taaluma.
UCHUMI WA VYOMBO VYA HABARI
Kuhusu hali ya uchumi katika vyombo vya habari amesema umekumbwa na changamoto kubwa katika mataifa mbalimbali akitolea mfano nchini Marekani ambako magazeti 3,200 yamefungwa na kuondoka sokoni.
Pia, magazeti yaliyokuwa yakipata faida ya mamilioni ya fedha sasa yanajiendesha kwa faida ndogo akitolea mfano kampuni ya Standard nchini Kenya.
“Kwa Tanzania kampuni kama New Habari iliweka historia kwa kujiondoa yenyewe sokoni. Takwimu sio nzuri sana kwa kuwa mapato yamepungua sio katika vyombo vya habari pekee, lakini hadi katika taasisi za habari na sisi Jukwaa la Habari tumekuwa na changamoto za kiuchumi na ndio maana hatujakutana kwa muda mrefu,” amesema.
Kutokana na hali hiyo ametoa rai kwa vyombo vya habari nchini kutafuta vyanzo vipya vya mapato badala ya kutegemea vilivyopo hasusan matangazo na mabaki ya magazeti.
Pamoja na hayo, kwa kipekee ametoa shukrani za dhati kwa niaba ya jukwaa hilo kwa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) kutokana na kuendelea kuliunga mkono jukwaa la Wahariri.
“Kwa kipekee tunaishukuru WCF kwa kuendelea kutuamini siku hadi siku na wamekuwa wakituwezesha kwa kiwango kikubwa kwa mfano kama walianza kutuchangia kwa sh. milioni tano wakaongeza milioni 10, milioni 15, hadi Sh. milioni 30. Kwa hiyo kwa kipekee tunaishukuru WCF kwa kuendelea kuwa nasi wakati wote.” amesisitiza.
Lengo la kikao hicho ni kujadiliana kuhusu masuala mbalimbali yanayolenga kuimarisha uhusiano na itikadi za vyama hivyo.
Na Mwandishi wetu
Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola ambaye pia ni Rais wa zamani wa Malawi, Mhe. Lazarus McCarthy Chakwera ameondoka nchini Aprili 16, 2026, kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) na kuagwa na viongozi waandamizi wa serikali wakiongozwa na Balozi wa Tanzania nchini Uingereza, Mhe. Mberwa Kairuki, baada ya kumaliza ziara yake ya kikazi ya siku 9 nchini Tanzania.
Mhe. Chakwera ambaye aliwasili nchini Aprili 8, 2026 kwa ziara ya kikazi, alikutana na kufanya mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Mawaziri akiwemo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo pamoja na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - Sera, Bunge, Uratibu Wenye Ulemavu, Prof. Palamagamba Kabudi ambaye aliongoza ujumbe wa Serikali kukutana na Mjumbe huyo Maalum.
Katika kikao na ujumbe wa Serikali, Mhe. Profesa Kabudi alimueleza kwa kina Mhe. Chakwera, kuhusu hatua mbalimbali zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuimarisha demokrasia nchini huku ikiweka msisitizo katika kulinda na kuheshimu utu wa Mtanzania, kuzingatia haki na uwajibikaji, amani na utulivu pamoja na kudumisha umoja wa kitaifa.
Kikao hicho na Mjumbe huyo Maalum kilikuwa chenye mafanikio baada ya Mhe. Chakwera kuelezwa namna serikali inavyoendelea kuchukua hatua mbalimbali hususani katika kudumisha amani, umoja wa kitaifa na ustawi wa Watanzania na kuhakikisha nchi inaendelea kuwa tulivu na kumuwezesha kila Mtanzania kushiriki kikamilifu katika kujenga uchumi jumuishi na kujiletea maendeleo.
Mbali na kukutana na ujumbe wa Serikali, Mheshimiwa Chakwera alifanya mazungumzo na Msajili wa Vyama vya Siasa, Mhe. Jaji Mstaafu Francis Mutungi, na pia vyama vya siasa vya ACT–Wazalendo, Chama cha National League for Democracy (NLD), United Democratic Party (UDP), Chama cha National Reconstruction Alliance (NRA), Chama cha NCCR Mageuzi, Chama cha Sauti ya Umma (SAU), Chama cha Alliance for Democratic Change (ADC), Alliance for African Farmers Party (AAFP) na Chama cha ADA-TADEA.
Vyama vingine ni pamoja na Democratic Party (DP), Tanzania Labour Party (TLP), Union for Multiparty Democracy (UMD), United People’s Democratic Party (UPDP), Chama cha Kijamii (CCK), Demokrasia Makini, Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMA) na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).
Mjumbe huyo Maalum pia alikutana na wadau mbalimbali akiwemo Mwenyekiti wa Tume ya Uchunguzi wa matukio yaliyotokea Oktoba 29, 2025 na baada ya Uchaguzi Mkuu, Jaji Mkuu Mstaafu Mhe. Mohamed Othman Chande, Waziri Mkuu Mstaafu na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jaji Joseph Warioba, Jumuiya zisizo za Kiserikali, Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar, Mhe. Jaji George Joseph Kazi, Mwenyekiti wa ACT – Wazalendo Mhe. Othman Masoud Othman, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Mussa Azzan Zungu, Jaji Mkuu wa Mahakama ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Jaji George Mcheche Masaju, Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele na Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi Mhe. Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro.
Akiwa nchini, Mhe. Chakwera alipata fursa ya kujionea namna Tanzania ilivyowekeza katika sekta ya usafiri ambapo wakati akienda Zanzibar kukutana na viongozi wa kisiasa kisiwani humo, alitumia usafiri boti ya kisasa inayofanya safari zake katika ya Dar es Salaam na Unguja, wakati akielekea Dodoma alitumia usafiri wa treni ya mwendokasi (SGR) na kufurahia namna Serikali ilivyowekeza na kuimarisha sekta ya usafiri nchini.
Ziara ya Mhe. Chakwera imekuwa ya mafanikio na kuionesha Afrika na dunia hali ya Amani na utulivuza iliyopo nchini Tanzania, licha ya changamoto zilizojitokeza wakati na baada ya uchaguzi mkuu, na namna ambavyo Serikali imeendelea kuchukua hatua madhubuti za kushughulikia changamoto hizo huku ikisimamia misingi ya kuimarisha demokrasia, Amani, utulivu na kuhakikisha kila mtanzania anashiriki vema katika kujenga uchumi na kuifikia Dira 2050 ambapo ifikapo mwaka 2050, Tanzania inalenga kuwa na uchumi wa dola za Marekani trilioni 1, huku kipato cha mtu mmoja mmoja kikizidi dola za Marekani 7,000.
Katika ziara yake hiyo, Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola aliwezeshwa kukutana na wadau wote aliohitaji kukutana nao pamoja na wale wote walioainishwa na Sekretarieti ya Jumuiya ya Madola.
Katibu wa NEC Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Kenan Kihongosi amesema siasa ni hesabu na wao wamekuwa wakishinda siku zote kwa sababu ya idadi kubwa ya wanachama walionayo.
Kihongosi ameeleza hayo leo Aprili 16,2026 alipotembelea na kuzungumza na wananchi na wanachama wa shina namba 12 Tawi la Bugulula Kata ya Bugulula wilaya ya Geita Vijijini mkoani Geita ikiwa ni muendelezo wa ziara yake katika mikoa ya Kanda ya Ziwa.
Akizungumza hayo Kihongosi amesema ukiangalia idadi kubwa ya watu waliopo hapo katika Shina namba 12 ni 200 kwa kudaria na Wilaya hiyo ina jumla ya mshina 3,614 na kuzidisha na idadi ya shina hilo moja unapata idadi kubwa ya watu.
“Ukiangalia idadi ya watu hapa, wanakadiriwa kuwa kama mia mbili katika shina moja, ukizidisha kwa mashina yote, unapata idadi kubwa sana ya watu, alafu kuna mtu anauliza sisi tutashindaje? Mwambie tunashinda kwa sababu tuna watu hawa ndio msingi wetu.
Ameongeza; “Siasa ni hesabu, vyama vingine vinawezaje kushinda kama havina watu, anashinda vipi bila idadi hii haiwezekani. Sisi tunaenda kwa namba, tunaenda kwa hesabu”.
Amesema hiyo ndiyo nguvu ya CCM kama chama wanaisimamia serikali kuhakikisha miradi inatekelezwa. wanakagua, wanaripoti kwa viongozi wa juu, na kama mambo ni mazuri yanaonekana, kama ni mabaya, wananchi wanafahamu.
Amesiaitiza tofauti na vyama vingine ni kwamba vinawahamasisha watu kupigana na kufanya vurugu, lakini watu wa Bugulula wanachotaka ni maendeleo wanahitaji barabara, umeme, shule, hospitali na pembejeo za kilimo, kwani hayo ndiyo mambo ya msingi.
“Lakini Mtu anakuja anasema kamanda, pambana, zungusha Wewe unapigana na nani? Msijidanganye, hakuna faida ya vurugu mimi nasema watu waandamane kutafuta pesa hayo ndiyo maandamano mazuri baba ukirudi nyumbani na hela, chakula au mazao, familia yako inanufaika,” amesema Kihongosi.
Na Janeth Raphael - MichuziTv
Tanzania imeweka historia mpya katika sekta ya afya baada ya kuwa mwenyeji wa Mkutano wa Kimataifa wa Shirikisho la Jumuiya ya Madaktari wa Upasuaji wa Ubongo, mkutano ambao ni wa pili kufanyika duniani na wa kwanza barani Afrika.
Akifungua mkutano huo jijini Dar es Salaam, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, alisema hatua hiyo inaonesha heshima kubwa kwa nchi na pia kuimarika kwa nafasi ya Tanzania katika huduma za afya za kibobezi.
Alibainisha kuwa mkutano huo unafuata ule wa kwanza uliofanyika Februari 2024 huko Peshawar, Pakistan, akisisitiza kuwa kufanyika kwake Afrika kwa mara ya kwanza ni hatua muhimu kwa bara hilo na kwa Tanzania kama mwenyeji.
Rais Samia alieleza kuwa upasuaji wa neva ni mojawapo ya fani nyeti na ngumu zaidi katika tiba, inayohusisha kuokoa maisha na kurejesha matumaini kwa wagonjwa wenye majeraha ya ubongo, uvimbe na matatizo ya uti wa mgongo. Alisisitiza kuwa magonjwa hayo yanahitaji utaalamu wa juu, umakini na kujitolea kwa wataalamu wa afya.
Aidha, alieleza kuwa serikali inatambua umuhimu wa sekta ya afya katika maendeleo ya taifa, na inaendelea kuwekeza katika huduma za kibobezi ili kuboresha ustawi wa wananchi. Alisema taifa lenye afya bora ni msingi wa ukuaji wa uchumi, uzalishaji na utulivu wa kijamii.
Katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, Tanzania imepiga hatua kubwa katika kuimarisha huduma za upasuaji wa neva. Idadi ya hospitali zinazotoa huduma hizo imeongezeka kutoka 2 mwaka 2020 hadi 7 kufikia Aprili 2026, hatua inayoonesha maboresho makubwa ya miundombinu na rasilimali watu.
Vilevile, idadi ya madaktari imeongezeka, ambapo madaktari wa upasuaji kwa ujumla wameongezeka kutoka 1,038 mwaka 2020 hadi 1,518 mwaka 2026. Madaktari wa upasuaji wa neva nao wameongezeka kutoka 12 hadi 37, ambapo 7 kati yao ni wanawake, hali inayoonesha kuimarika kwa ushirikishwaji wa kijinsia katika fani hiyo.
Katika upande wa teknolojia, serikali imeongeza uwekezaji katika vifaa tiba ambapo mashine za MRI zimeongezeka kutoka 7 hadi 14, CT scan kutoka 12 hadi 97, na X-ray za kidijitali kutoka 147 hadi 457, hatua inayolenga kuongeza ubora na upatikanaji wa huduma za uchunguzi.
Serikali pia imeeleza kuendelea kuimarisha sekta ya afya kupitia mafunzo ya wataalamu, uboreshaji wa miundombinu na teknolojia, upanuzi wa huduma za telemedicine, utekelezaji wa bima ya afya kwa wote, ushirikiano kati ya sekta binafsi na serikali pamoja na uboreshaji wa mifumo ya kidijitali ya afya kama GOTHOMIS.
Mkutano huo unaendelea kujadili maendeleo na mustakabali wa huduma za upasuaji wa neva duniani, huku Tanzania ikitumia fursa hiyo kuonesha mafanikio yake na kuimarisha ushirikiano wa kimataifa katika sekta ya afya.









.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)





















