NA MASHAKA MHANDO, Handeni

WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, amemwagiza Katibu Mkuu Wizara ya elimu, sayansi na teklonojia, kuwachukulia hatua watumishi wa Wizara hiyo waliosimamia ujenzi wa Chuo Cha Veta wilayani hapa na kusababisha mifuko 1,262 ya saruji kuganda.

Sambamba na agizo hilo Waziri Mkuu pia amemwagiza Kamanda wa Takukuru  mkoani Tanga, kwenda kufanya uchunguzi wa matumizi mabaya ya fedha katika jengo la kituo cha afya Sindeni ambako milango 34 ipo chini baada ya mkandarasi kuweka milango hiyo kwa kiwango cha chini.

Akizungumza jana jioni katika ziara yake ya siku ya kwanza mkoani hapa, Waziri Mkuu amemwagiza Mkuu wa mkoa kufuatilia la matumizi mabaya ya fedha kwenye miradi hiyo ambayo.

Alisema wilayani Handeni kuna miradi imekuwa na kasoro ambapo jengo la mama na mtoto katika kituo cha afya Sindeni milango ipo chini ya kiwango kutokana na watu kufanya kazi kwa mazoea.

"Kamanda wa Takukuru wote waliohusika wachukuliwe hatua za kisheria, RC (Mkuu wa mkoa Balozi Dkt Batilda Burihan) Fuatilia wahusika wote kama wameweka milango hiyo kusudi ili wachukue fedha za serikali, wachukuliwe hatua mradi ule ni wa zaidi ya milioni 300," alisema Waziri Mkuu.

Pia Waziri Mkuu ametaka watumishi ambao wamesimamia ujenzi wa maabara ya Chuo Cha Veta wilayani hapa ambao wamesababisha mifuko hiyo ya saruji kuganda wahakikishe wanarudisha fedha hizo na kama walifanya uzembe wachukuliwa hatua.

"Waliotumwa kujenga Veta ili vijana wasome wamekaa ofisini wakagandisha mifuko 1,262, huu ni uzembe tunasema hatuwezi kuvumilia, nimekuja hapa nikijua ni halmashauri mmefanya hivyo lakini nimeambiwa je go Hilo linasimakiwa na watumishi wa Wizara ya elimu, namwagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya elimu awavhukulie hatua na wakatwe fedha kwenye mishahara yao kurejesha ili jengo hilo lijengwe," alisema.

Waziri Mkuu alisema kuwa Sasa watumishi wa serikali waache kufanya kazi kwa mazoea na badala yake wafanye kazi kuwahudumia watanzania ambao wamekuwa na matumaini makubwa na serikali yao.

Awali wakati akikagua eneo la ujenzi wa kituo cha kupozea Umeme eneo la Mkata,  ameiagiza Wizara ya Fedha kuhakikisha inatoa kiasi cha Shilingi Bilioni 1.9 zilizobaki kwa ajili ya mkandarasi anayejenga kituo cha kupozea umeme (Substation) mjini Mkata, ili mradi huo ukamilike kwa wakati.

Akizungumza mara baada ya kukagua mradi huo na kupata taarifa kutoka kwa Mtendaji Mkuu wa TANESCO, Mhandisi Lazaro Twange, Waziri Mkuu amesema kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imetoa fedha kwa ajili ya miradi ya umeme ili kuongeza upatikanaji wa Nishati hiyo ipatikane kwa wananchi na wawekezaji.

Ameagiza Wizara ya Nishati, chini ya Waziri Deogratius Ndejembi, kufuatilia kwa ukaribu utoaji wa fedha hizo ili mkandarasi aongeze kasi ya ujenzi, kwani mradi huo ni sehemu ya uwekezaji wa Trilioni Moja zilizotolewa nchi nzima unaolenga kuboresha nishati kwa ajili ya viwanda.

Alisema Rais Dkt Samia Suluhu Hassan ameonyesha uungwana na vitendo kwa kutekeleza ahadi zake mapema, katika siku zake 100 za uongozi wake  ikiwemo ajira za watumishi 5,000 wa afya na 7,000 wa elimu ndani ya kipindi kifupi.

Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu ametoa onyo kali kwa wakandarasi wanaochepusha fedha za miradi kwenda kulipa madeni yao binafsi au kwenye miradi mingine, akisisitiza kuwa Serikali haina mzaha katika suala hilo. 

"Tunataka kiasi cha fedha kilichopokelewa kilingane na thamani ya kazi iliyofanyika. Kuna wakandarasi wanatoa namba za akaunti zao za nje ambazo zina madeni, wakilipwa fedha zinakatwa na benki na mradi unakwama. Watu wa aina hiyo wachukuliwe hatua za kisheria mara moja," alisisitiza Waziri Mkuu.

Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, amebainisha kuwa Serikali ya Awamu ya Sita imetoa jumla ya Shilingi Trilioni 1.9 kwa ajili ya kutekeleza miradi mikubwa ya umeme ipatayo 27 nchi nzima, ukiwemo mradi huu wa Mkata unaolenga kuimarisha upatikanaji wa nishati kwenye Gridi ya Taifa.

Waziri Ndejembi alisisitiza kuwa ujenzi wa kituo hicho cha kupozea umeme (Substation) ni suluhisho la kudumu kwa wawekezaji, hususan wa viwanda vya madini ya Graphite, ambao hapo awali walikuwa wakisita kuwekeza kutokana na changamoto ya nishati. 

"Rais ametoa Trilioni 1.9 kwa ajili ya miradi hii 27 ya umeme nchini. Hapa Mkata tunapeleka umeme wa uhakika kutoka Bwawa la Mwalimu Nyerere, na tayari Bilioni 3 zimetolewa kwa ajili ya kubadilisha nguzo za umeme kuelekea Kwamsisi ili kuimarisha miundombinu hiyo,"* alisema Waziri Ndejembi.

Aidha, Waziri huyo wa Nishati ameahidi kuwasimamia kwa karibu wakandarasi wote ili kuhakikisha kazi hizo zinakamilika kwa wakati uliopangwa, akisisitiza kuwa kukamilika kwa miradi hiyo kutafungua fursa mpya za kiviwanda na kiuchumi kwa mkoa wa Tanga na maeneo jirani.

Mtendaji Mkuu wa TANESCO amebainisha kuwa Serikali inaendelea na uimarishaji wa Gridi ya Taifa mkoani Tanga kupitia miradi miwili mikubwa. Mradi wa Mkata unahusisha ujenzi wa kituo cha kupoza umeme (2X60MVA) na njia ya kilomita 45 kuelekea Kwamsisi.

Mradi huu unagharimu Shilingi Bilioni 49.89 na unatekelezwa na kampuni ya TBEA kutoka China na Central Electricals ya Tanzania kwa lengo la kuimarisha nishati kwenye migodi ya Graphite na viwanda.

Hadi kufikia Februari 2026, ujenzi wa kituo cha Mkata umefikia asilimia 20.37, huku kazi za misingi zikiwa zimekamilika kwa asilimia 55. Kwa upande wa njia ya usambazaji, tayari nguzo zimeshasimikwa kwa urefu wa kilomita 30 kati ya 45 zinazohitajiwa.

Sambamba na hayo, Serikali inatekeleza mradi mwingine wa kimkakati wa "Gridi Imara" kutoka Mkata hadi Kilindi (kV 132) wenye urefu wa kilomita 143.6. Mradi huu unatekelezwa na kampuni ya Kalpataru kutoka India kwa gharama ya Shilingi Bilioni 98.46.

Mpaka sasa, ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme Kilindi umefikia asilimia 30.9 na kituo cha kupoza umeme asilimia 35.9, huku ununuzi wa mitambo ukiwa umekamilika kwa asilimia 80.

Akijibu kero ya wananchi kuhusu migogoro ya ardhi kati ya wakulima na wafugaji, Dkt. Mwigulu amewataka Watanzania kuacha kubaguana na badala yake wafuate sheria za nchi zinazoruhusu Mtanzania kuishi popote bila kuvunja taratibu.

Waziri Mkuu amebainisha mambo makuu mawili ambayo ni Mtanzania anaruhusiwa kuishi popote, lakini lazima azingatie Sheria akitambuabkuwa ardhi haiongezeki wakati idadi ya watu inaongezeka.

Lakini pia alisema  kosa la mfugaji mmoja au mkulima mmoja lisiwakilishe jamii nzima bali wananchi waishi kwa kuheshimiana ili kuepusha migongano isiyokuwa na lazima.

Alisema migogoro ya wakulima na wafugaji isifike wakati ikakosa Utu miongoni mwa jamii hizo hivyo akataka waheshimiane na utatuzi wa migogoro ambayo inatakiwa iamuliwe kwa mujibu wa  Sheria.

 "Tuambizane na tuchukue hatua haya mambo tukiyaacha yataleta ufa miongoni mwetu, tuchukue mkondo wake kwa mtu binafsi anayevunja sheria na siyo kuanzisha ufa wa utengano," alisema.

Amewaagiza viongozi wa Kamati ya Ulinzi na Usalama mkoani Tanga kutofumbia macho rushwa inayochelewesha haki na badala yake wasimamie matumizi bora ya ardhi ili kumaliza mizozo hiyo kwa uungwana.

Waziri Mkuu amesikiliza kero za wananchi nyingine alizitatua papo hapo na nyingine ameagiza mawaziri wa Wizara za kisekta wakae pamoja kupata masuluhisho ya majawabu ya wananchi.

Katika ziara hiyo Waziri Mkuu alikuwa na waziri wa Kilimo Daniel Chongolo ambaye alisema wilayani Handeni ili migogoro ya wakulima na wafugaji iweze kuondoka wameandaa mpango wa matumizi Bora ya ardhi kwa kushirikiana na wizara za Mifugo na ardhi ili kutenga na kuhakikisha makundi hayo yanaishi kwa Amani.

Pia alisema wananchi wa Handeni katika Msimu wa chakula waliweza kulima ufuta, mbaazi na dengu na kupata jumla ya shilingi bilioni 2.7 na kwamba Sasa mpango uliyopo ni kujenga mabwawa ya umwagiliaji katika vijiji sita wilayani humo.

Naye Waziri wa Mifugo na Uvuvi Balozi Dkt Bashiru Ally Kakurwa alisema kuwa yote yaliyoainishwa katika ilani ya CCM ya mwaka 2025-2030 yatatekelezwa ikiwemo kuweka mpango wa uzalishaji wa mbegu bora za Mifugo na ambari.

Pia alisema kuboresha afya ya Mifugo kwa kutoa chanjo ambayo Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kuzindua chanjo hizo mwaka jana lakini pia kuboresha sekta ya Uvuvi kwa serikali kununua boti tano na moja itawasili February 21.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na serikali za mitaa Tamisemi Profesa Rizik Shemdoe alisema wanamshukuru Rais kwa kuwapatia miradi ya kimkakati katika mkoa wTanga ikiwemo ujenzi wa Majengo ya dharura katika hospitali za wilaya ya Handeni, Pangani na Korogwe.

Mbunge wa Handeni mjini Reoben Kwagwila na Naibu Waziri wa Tamisemi alisema kutoka na furaha ya kupata maji kutokana na mradi mkubwa wa miji 28 ambao itafika wilayani hapa, siku ya uzinduzi ataoga hadharani kutokana na furaha ya kupata maji na kukosa muda mrefu.

Waziri wa maji Jumaa Aweso alisema kuwa jumla ya shilingi bilioni 171 zinagharamia mradi wa Maji wa miji 28 ambao ni katika wilaya za Korogwe, Handeni, Muheza na Pangani hivi Sasa umefikia asilimia 75 na kwamba hadi kufikia Machi mwaka huu maji yataanza kupatikana matika maeneo hayo.









 

-Azitaka nchi za Afrika kuunganisha nguvu

-Wajumbe wamsifu Rais Samia kwa kuwa kinara


Na John Mapepele- Addis Abbaba. 

Waziri wa afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa  amesema Afrika inatakiwa kuunganisha nguvu katika kuweka mikakati ya pamoja  katika kupunguza  vifo vya mama  na mtoto ili kuondokana na  changamoto  hiyo.

Mhe. Mchengerwa ametoa kauli hiyo leo Februari 13, 2026 jijini Addis Abbaba nchinini Ethiopia   kwenye  mkutano wa Nchi zote za Umoja wa Afrika wakati anafungukua mkutano huo, akimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania , Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mhe. Mchengerwa amesema Umoja wan chi za Afrika umeipa Tanzania heshima kubwa  ya kufungua mkutano huo kwa kutambua juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali ya Tanzania ikiongozwa na Rais, Samia Suluhu Hassan  katika kupunguza kwa kasi vifo  vya mama na mtoto  wakati wa kujifungua.

“Ni ukweli usiopingika kuwa Rais Samia amefanya kazi kubwa sana  katika eneo hili la kupunguza  vifo vya mama na mtoto katika kipindi kifupi na kupata tuzo nyingi, na  ndiyo sababu wameipatia nchi yetu hesghima  ya kufungua  mkutano huu mkubwa”.Amefafanua Mhe. Mchengerwa

Mkutano  huu umehudhuliwa  na takribani nchi zote za Afrika ambapo mawazari wa Afya wa nchi hizo wamepata fursa ya kufanya majadiliano ya namna bora  ya kukabiliana na  changamoto ya vifo vya mama na mtoto huku Tanzania ikipigiwa mfano wa kufanya vizuri katika eneo hili.

Aidha, wajumbe  wameonyesha kuridhishwa na hatua zinazochukuliwa  na nchi  wanachama  na kwamba kumekuwa na mafanikio yanayoonekana kupitia kampeni ijulikanayo kama CARMMA (2021- 20300 chini ya Umoja wa Nchi za Afrika inayolenga  kupunguza  vifo  vya mama na mtoto.

Mkutano huu unafanyika jijini Addis Ababa nchini Ethiopia pembezoni mwa Mkutano wa 39 wa Wakuu wa Nchi wa Umoja wa Afrika unaofanyika kesho na kesho kutwa ambapo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan anashiriki na amependekezwa kuwa kinara wa Umoja wa Afrika katika Masuala ya   Afya ya Mama na Mtoto, uteuzi ambao unatarajiwa kupitishwa rasmi na Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali.







 

Na Mwandishi Wetu 

Tume ya Ushindani (FCC) imesema kufuatia taarifa za kiintelijensia katika soko la Kariakoo ilifanya operesheni ya ukamataji   wa vilainishi bandia vya magari vilivyokuwa na alama za biashara zinazomilikiwa bila ridhaa za wamiliki wa alama hizo. 

Katika taarifa iliyotoelwa na Kitengo cha Mawasiliano na Mahusiano ya Umma

Tume ya Ushindani (FCC)   imesema operesheni hiyo ilifanyika  katika eneo la Kariakoo, Mtaa wa Udoe, Wilaya ya Ilala, Dar es Salaam na kukamata madumu zaidi ya 5,000 yenye ujazo tofauti wa vilainishi yanashukiwa kuwa bandia,mashine tatu za uzalishaji/ujazaji upya pamoja na  stika za chapa  bandia

Bidhaa na vifaa vyote vilivyokamatwa vimehifadhiwa kama vielelezo, vikisubiri uthibitisho kutoka kwa wamiliki wa alama za bidhaa husika.

Kwa mujibu wa taarifa ilisema ukamataji wa vilainishi hivyo vya magari vinavyoshukiwa kuwa bandia ulifanyika  kwa  mujibu wa sheria

FCC inatoa rai kwa wafanyabiashara kutojihusisha na utengenezaji, usambazaji, au uuzaji wa bidhaa bandia ya aina yoyote ikiwemo vilainishi vya magari vina madhara makubwa ikiwemo kuharibu injini, kusababisha hasara ya kifedha, na kuhatarisha usalama. 

Hata hivyo  wafanyabiashara na umma kwa ujumla kufahamu kwamba bidhaa bandia huhatarisha usalama wa maisha, mali na afya za walaji na zina athari kubwa kwa biashara halali na uwekezaji 

 nchini kwani zinaleta ulingo usio sawa katika biashara .

FCC inawahimiza wananchi kutoa taarifa FCC kuhusu uwepo wa shughuli zinazohusiana na bidhaa bandia kupitia simu ya bure 0800 11 00 94 au info@fcc.go.tz kwa ajili ya kuchukua hatua stahiki kwa mujibu wa Sheria ya Alama za Bidhaa. Kwa pamoja tunaweza kuifanya Tanzania kuwa salama bila ya bidhaa bandia.

Na Karama Kenyunko Michuzi Tv 

NAIBU Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidhi Amir, amewataka vijana kuchangamkia fursa za mikopo inayotolewa kupitia Mfuko wa Samia wa Ubiasharishaji Ubunifu ili waweze kutimiza ndoto zao na kujikwamua kiuchumi.

Aidha, amesikitishwa na idadi ndogo ya wabunifu waliojitokeza kuomba mkopo huo, huku akiitaka Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) pamoja na Benki ya CRDB, wanaosimamia utekelezaji wa mfuko huo, kuendelea kutoa elimu kwa vijana ili wengi zaidi wanufaike.

Wanu ameyasema hayo leo, Februari 13, 2026 jijini Dar es Salaam wakati akifungua warsha ya siku moja ya kuwajengea uwezo wabunifu na kuwatambua wanufaika wa mfuko huo. Amewahimiza vijana kutuma maombi kwa kuwa fedha zipo na hazijatumika ipasavyo.

Amesema katika kipindi cha miezi kumi, vijana saba pekee ndio walionufaika na mkopo wa jumla ya Sh milioni 767 kati ya Sh bilioni 4.6 zilizotengwa kwa ajili ya mfuko huo.

“Kwa idadi kubwa ya wabunifu tulionao nchini, matarajio yangu yalikuwa fedha hizi zingeshachukuliwa ndani ya mwaka mmoja. Nimeambiwa baadhi walikwama kutokana na kukosa taarifa sahihi au kutokukidhi vigezo vya kibiashara,” amesema Wanu.

Kutokana na changamoto hizo, ameagiza zifanyiwe kazi kwa kuandaliwa mafunzo maalum yatakayowawezesha wabunifu kupata uelewa na uwezo wa kukidhi masharti ya mkopo.

“Nitoe wito kwa COSTECH na CRDB kuendelea kuwapa elimu wabunifu. Kama kuna changamoto za kimfumo, zipatiwe ufumbuzi wa haraka ili fedha hizi ziwanufaishe walengwa kama ilivyokusudiwa,” amesisitiza.

Akinukuu taarifa ya Mkurugenzi wa CRDB, Wanu amesema vijana wenye uhitaji ni wengi, hivyo ni muhimu kubaini vikwazo vinavyowafanya wasifikie fursa hiyo, hasa ikizingatiwa kuwa fedha zilizotolewa hazijafikia hata asilimia 10 ya kiasi kilichopo.

Amewahimiza vijana wenye ubunifu wa bidhaa au utoaji huduma kuendelea kuwasilisha maombi kupitia COSTECH na wasikate tamaa hata kama fomu zina maswali mengi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH, Dkt. Amos Nungu, amesema mfuko huo wenye thamani ya Sh bilioni 4.6 hadi sasa umepokea maombi 100. 

Kati ya hayo, maombi 22 yamekamilika, 15 hayakukidhi vigezo vya kibiashara, na saba ndiyo yalikidhi vigezo. Wabunifu watatu tayari wamepokea fedha zao huku wanne wakiwa katika hatua za mwisho za kupatiwa mikopo.

Dkt. Nungu amesema lengo la mfuko huo ni kuwawezesha vijana wabunifu kupata mitaji, kukuza biashara zao na kurejesha mikopo ili fedha ziendelee kuwanufaisha wengine.

Mmoja wa wanufaika, Poul Musiba, ambaye kampuni yake inajihusisha na ufugaji wa nyuki, ameishukuru serikali kwa fursa hiyo. Amesema alipata mkopo wa Sh milioni 135 kati ya Sh milioni 200 alizoomba, hatua iliyomsaidia kupanua shughuli zake za uzalishaji.









Azitaka nchi za Afrika kuunganisha nguvu

Wajumbe wamsifu Rais Samia kwa kuwa kinara

Na John Mapepele- Addis Abbaba. 

Waziri wa afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa  amesema Afrika inatakiwa kuunganisha nguvu katika kuweka mikakati ya pamoja  katika kupunguza  vifo vya mama  na mtoto ili kuondokana na  changamoto  hiyo.

Mhe. Mchengerwa ametoa kauli hiyo leo Februari 13, 2026 jijini Addis Abbaba nchinini Ethiopia   kwenye  mkutano wa Nchi zote za Umoja wa Afrika wakati anafungukua mkutano huo, akimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania , Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mhe. Mchengerwa amesema Umoja wan chi za Afrika umeipa Tanzania heshima kubwa  ya kufungua mkutano huo kwa kutambua juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali ya Tanzania ikiongozwa na Rais, Samia Suluhu Hassan  katika kupunguza kwa kasi vifo  vya mama na mtoto  wakati wa kujifungua.

“Ni ukweli usiopingika kuwa Rais Samia amefanya kazi kubwa sana  katika eneo hili la kupunguza  vifo vya mama na mtoto katika kipindi kifupi na kupata tuzo nyingi, na  ndiyo sababu wameipatia nchi yetu hesghima  ya kufungua  mkutano huu mkubwa”.Amefafanua Mhe. Mchengerwa

Mkutano  huu umehudhuliwa  na takribani nchi zote za Afrika ambapo mawazari wa Afya wa nchi hizo wamepata fursa ya kufanya majadiliano ya namna bora  ya kukabiliana na  changamoto ya vifo vya mama na mtoto huku Tanzania ikipigiwa mfano wa kufanya vizuri katika eneo hili.

Aidha, wajumbe  wameonyesha kuridhishwa na hatua zinazochukuliwa  na nchi  wanachama  na kwamba kumekuwa na mafanikio yanayoonekana kupitia kampeni ijulikanayo kama CARMMA (2021- 20300 chini ya Umoja wa Nchi za Afrika inayolenga  kupunguza  vifo  vya mama na mtoto.

Mkutano huu unafanyika jijini Addis Ababa nchini Ethiopia pembezoni mwa Mkutano wa 39 wa Wakuu wa Nchi wa Umoja wa Afrika unaofanyika kesho na kesho kutwa ambapo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan anashiriki na amependekezwa kuwa kinara wa Umoja wa Afrika katika Masuala ya   Afya ya Mama na Mtoto, uteuzi ambao unatarajiwa kupitishwa rasmi na Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali.


 


Na: OWM (KAM) - Dodoma

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Clement Sangu amezindua Programu ya Nchi ya Kazi za Staha Awamu ya Tatu ya Mwaka 2025/2026 – 2029/2030 na Mkakati wa kukuza Kazi za Staha Kwa wafanyakazi wa nyumbani.

Aidha, amesema Progamu hii inalenga kuimarisha majadiliano ya kijamii (social dialogue) na mshikamano baina ya Serikali, Waajiri na Wafanyakazi. Pia kuhakikisha wafanyakazi wa nyumbani wapata ulinzi, kutambuliwa na kufikiwa fursa wanazo stahili ili kuongeza kazi za staha.

Uzinduzi huo umefanyika leo Februari 13, 2026 katika ukumbi wa Hoteli ya Best Western, Jijini Dodoma

Vilevile, Waziri Sangu amesema serikali itaendelea kuwezesha mazingira wezeshi yatakayo rahisisha maendeleo ya programu za kazi za staha.

Kwa upande wake, Kamishna Mkuu wa Kazi, Suzan Mkangwa amesema Serikali ipo katika mchakato wa kuridhia mkataba wa wafanyakazi wa majumbani, hivyo kukamilika wa Programu ya Nchi ya Kazi za Staha Awamu ya Tatu utasaidia kufanikisha maridhiano ya mkataba huo.

Kadhalika, Kamishna Mkangwa amesema kuwa Serikali imeendelea kuwapatia kipaumbele wafanyakazi wa nyumbani kwa kusimamia maslahi yao na kuwalinda kupitia mifumo ya sheria ikiwemo Sheria ya Mahusiano Kazini ambayo inaainisha viwango vya kazi wote ikiwa ni Pamoja na wafanyakazi wa nyumbani.

Naye, Mkurugenzi Shirika la Kazi Duniani (ILO) Afrika Mashariki, Bi. Caroline Mugala, amesema kazi za staha ni utu hivyo jambo jema nchi wanachama wa ILO kuhakikisha wafanyakazi wanafanya kazi za staha kwa kuwa zinahakikisha haki katika maeneo ya kazi, kinga ya jamii na majadiliano mema katika maeneo ya kazi.

Ameongeza kuwa utekelezaji wa programu ya kazi za staha itaimarisha Maendeleo ya ukuaji wa uchumi wa Tanzania.


 

Na Mwandishi Wetu

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imesema utekelezaji wa mfumo wa ithibati kwa waandishi na watangazaji wa habari nchini ni hatua ya kimkakati ya kuimarisha uaminifu, weledi na ushindani wa sekta ya habari katika uchumi wa kisasa unaotegemea taarifa sahihi na zenye kuaminika.

Akizungumza katika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji (ABC) uliofanyika Februari 13, 2026 jijini Dodoma, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, amesema ithibati inalenga kujenga taaluma yenye misingi imara ya kitaaluma, maadili na uwajibikaji kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229.
Kwa mujibu wa Wakili Kipangula, ithibati si chombo cha kudhibiti maudhui, bali ni utaratibu wa kuweka viwango vinavyolinda hadhi ya taaluma na kuimarisha imani ya umma kwa vyombo vya habari na kwamba katika mazingira ya sasa ya ushindani wa kidijitali, uaminifu wa chanzo cha habari ndiyo mtaji mkubwa wa chombo husika.

Ameongeza kuwa vyombo vya utangazaji vinavyowekeza katika weledi wa rasilimali watu wake vinajiweka katika nafasi bora ya kuvutia wawekezaji, matangazo na ushirikiano wa kimataifa, kwa kuwa soko la habari linazidi kuthamini ubora na uwajibikaji.
Kwa upande wa wadau wa mkutano huo ulioandaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), imeelezwa kuwa ushirikiano kati ya msimamizi wa maudhui na wadau wa tasnia ni nguzo muhimu katika kujenga sekta imara, inayochochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Hatua ya kuimarisha ithibati inaonekana kuwa sehemu ya mkakati mpana wa Serikali wa kukuza taaluma za ubunifu na mawasiliano kwa viwango vinavyokidhi mahitaji ya kitaifa na kimataifa, huku ikihakikisha kuwa sekta ya habari inabaki kuwa mhimili wa uwazi, uwajibikaji na maendeleo endelevu.

Waandishi zaidi ya 3,200 kati ya 3,900 walioomba vitambulisho vya uandishi wa habari (Press Card) wamethibitishwa baada ya kukidhi vigezo vya kisheria, hali inayoonesha mwitikio chanya wa wadau na utayari wa sekta kujiimarisha kitaaluma.

Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Rahma Kisuo ameshiriki Mkutano wa 6 wa Kimataifa wa Kutokomeza Utumikishwaji wa Mtoto (6th Global Conference on the Elimination of Child Labour) uliofanyika kuanzia tarehe 11 hadi 13 Februari, 2026 Marrakech, Morocco.

Aidha, Mkutano huo umeandaliwa na Shirika la Kazi Dunia (ILO) ambalo limewaleta pamoja Mawaziri na wadau kutoka nchi mbalimbali duniani kwa lengo la kujadili na kukubaliana mikakati madhubuti ya kutokomeza utumikishwaji wa watoto ifikapo mwaka 2030.

Akiwa katika Mkutano huo, Naibu Waziri Kisuo alipata fursa ya kuwasilisha mafanikio ya Tanzania katika kukabiliana na Utumikishwaji wa Mtoto ambapo kiwango cha kimepungua kwa asilimia 9.1 kutoka asilimia 33.8 mwaka 2014 hadi asilimia 25.8 mwaka 2024, kwa mujibu wa Utafiti wa Watu wenye Uwezo wa Kufanya Kazi wa mwaka 2024.

Vilevile, Mhe. Kisuo alisema Serikali inaendelea kuimarisha ushirikiano na wadau wa maendeleo ili kuhakikisha watoto wote wanalindwa, wanapata elimu bora na fursa sawa za maendeleo.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe, Wanu Hafidhi Ameir amesema Serikali inaendelea na mchakato wa kufanyia maboresho ya Sheria ya elimu ili iende sambamba na mabadiliko ya Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 toleo la 2023 pamoja na maboresho ya mitaala.
 
Mhe. Wanu ameyasema hayo jijini Dar es salaam Februari 13, 2026 alipomuwakilisha Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda katika kikao cha Wadau wa Mtandao wa Elimu TEN/MET kutoa maoni ya mapitio ya sheria ya elimu, sura ya 353.

Amesema Utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo 2014, Toleo la 2023 unagusa ngazi zote za elimu na mafunzo hivyo, Wizara, pamoja na tathmini inayoendelea ya Sheria ya Elimu na sheria za Taasisi mbalimbali zilizo chini ya Wizara, inaendelea pia na mapitio ya miundo ya taasisi mbalimbali zilizo chini ya Wizara kwa lengo la kuleta tija na ufanisi katika utekelezaji wa Sera katika ngazi zote za elimu na mafunzo.

“Sote tutakubaliana kuwa uwepo wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya 2014, Toleo la 2023 ni jambo moja, lakini utekelezaji wake unahitaji nyenzo mbalimbali za kuiwezesha Sera yenyewe kutekelezeka. Nyenzo mojawapo ni kuwepo kwa Sheria ya Elimu iliyoboreshwa hvyo tunawashukuru kwa kuendelea kutoa maoni ya kuboresha sharia yetu ya elimu,” amesema Mhe. Wanu

Kwa upande wake Bi Martha Makala Mratibu Taifa Mtandao wa Elimu Tanzania (TEN/MET) amesema Mapitio ya Sheria ya elimu ya mwaka 1978   sura  ya 353 inatoa fursa ya kuijenga Tanzania yenye elimu jumuishi, haki, yenye ubora inayolinda watoto na wanafunzi katika kutatua changamoto ikiwemo ukosefu wa ajira

Ameipongeza Wizara kwa kutekeleza tamko la kisera la kushirikisha wadau  kwenye mchakato huo, hatua inayoongeza wigo wa kufanya kazi na wadau na kwamba wao kama Mtandao wamepata fursa ya kutoa maoni katika maeneo yanayohitaji maboresho  katika sheria ya Elimu ya Mwaka 1978.

Ameyataja maeneo hayo kuwa ni wanafunzi  kukatisha masomo, kuwepo kifungu cha sheria kinachoeleza bayana kuhusu wanafunzi waliokatisha masomo kuhakiksha wanamaliza mzunguko wao wa masomo ili kuwa na undelevu wa kuwarejesha walioacha masomo,

Elimu ya lazima miaka 10 iwekwe kisheria ili kuwa endelevu,elimu bila  ada iwekwe kisheria ili kuwa na uendelevu, lishe shuleni wazazi na walezi iwekwe kisheria  ili kuongeza uwajibikaji  kwa baadhi ya wazazi na walezi, kufanyika marekebisho ya sheria kwa ajili ya  kuondoa ukinzani uliopo kwenye sheria ya ndoa na sheria itakayohakikisha uendelevu wa Bodi ya kitaaluma ya walimu.

Nae Mwenyekiti wa Kamati ya Mapitio ya Sheria ya Elimu ya mwaka 1978 Prof. Saudin Mwakaje amesema mapitio ya sheria hayo yanalenga kuimarisha mifumo ya kijamii na kiuchumi na kukidhi  mahitaji ya mabadiliko mapya  hususani utekelezaji wa mikataba ya kimataifa na uhalisia wa soko la ajira.   

Wakichangia maoni yao kuhusu uboreshaji wa sheria ya elimu, wadau wameiomba Wizara kuangalia upya suala la muda wa masomo ya ziada (tuition) wakisema  baadhi ya walimu hutumia muda wa vipindi vya ziada kufundisha mada ambazo zingepaswa kufundishwa darasani, hali inayowaweka katika mazingira magumu wanafunzi wasioweza kuhudhuria vipindi hivyo. 

Pia  wamependekeza lugha ya alama ifundishwe kuanzia shule za msingi hadi vyuo vikuu, ili kurahisisha mawasiliano, hususan katika maeneo muhimu ya huduma za jamii kama hospitali na masoko.

Kadhalika, wadau wamependekeza shule mpya za sekondari zinazojengwa nchini ziwe na majengo ya mabweni, hatua itakayosaidia kulinda watoto wa kike dhidi ya vishawishi mbalimbali na kuongeza usalama pamoja na ufanisi wao katika masomo.












Top News