Chama cha Mapinduzi (CCM) kimewahimiza wananchi wa Wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma kuendelea kuitunza na kuilinda amani iliyopo, huku kikiwaonya kutokubali kushawishiwa kuivuruga kwa maslahi ya watu wasioitakia mema Tanzania.

Wito huo umetolewa leo ljumaa, Februari 20, 2026 na Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM, Kenani Labani Kihongosi, alipokuwa akitembelea na kukagua uhai wa shina namba tano la Chama Cha  Mapinduzi katika eneo la Kasangezi, wilayani Kasulu, mkoani Kigoma.

Akizungumza na wanachama na wananchi wa eneo hilo, Kihongosi alirejea historia ya Mkoa wa Kigoma kuhifadhi wakimbizi kutoka nchi jirani zinazokumbwa na machafuko, akisema hali hiyo inadhihirisha kuwa Tanzania ni kisiwa cha amani kinachopaswa kulindwa kwa gharama zote.

"Msidanganywe na watu wanaotaka kuwalaghai mkaharibu amani ya hapa Kasulu. Hakuna shida kubwa kama kutangatanga katika nchi za watu. Msikubali kushawishiwa kufanya vurugu au mambo yatakayovuruga utulivu wenu. Lindeni amani ya hapa kwenu," amesema Kihongosi.

Ameongeza kuwa wananchi wanapaswa kuwa makini na wanasiasa au watu wanaochochea vurugu, akidai kuwa mara nyingi wanaochochea migogoro hawaishi katika maeneo husika wala hawaguswi moja kwa moja na athari zake.











*Ni za wakulima wa kahawa AMCOS ya Mwika Kinyamvuo

*Akagua ujenzi wa hospitali ya Halmashauri ya Manispaa ya Moshi

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amemuagiza Mrajisi wa Vyama vya Ushirika mkoa wa Kilimanjaro ahakikishe Chama cha Ushirika Mkoa wa Kilimanjaro (KNCU) kinalipa kwa mkupuo mmoja sh. milioni 400 ambazo chama hicho kinadaiwa na wakulima.

Ametoa agizo hilo leo (Ijumaa, Februari 20, 2026) aliposimama kusalimia wananchi katika eneo la Chekereni ambapo mkazi wa eneo hilo, Bi. Glory Sam kutoka Chama cha Mwika Kinyamvuo AMCOS alieleza malalamiko yake mbele ya Waziri Mkuu akitaja kusikitishwa na KNCU kuuza kahawa yao msimu wa mwaka 2021/2022 lakini hadi sasa hawajalipwa.

“Tuliuza kahawa yetu kwa zaidi ya shilingi milioni 600 lakini mpaka sasa tumelipwa shilingi milioni 200 pekee. Kwa kipindi chote hicho tumekuwa tukidai milioni 400 bila mafanikio.”

Dkt. Mwigulu amemtaka Mrajis ahakikishe kuwa hadi kufikia tarehe 25 Februari, 2026 Bodi hiyo iwe imekaa kikao na iamue ni mali gani zinauzwa ili kuweza kuwalipa kwa mkupuo wakulima hao.

“Tafuta kimojawapo kiuzwe, shilingi milioni 400 ipatikane na hawa watu walipwe mara moja.  Hatuwezi kukaa na jambo moja miaka yote, kama kuna chama hakiwezi kulipa watu mnakaa nacho cha nini? Wananchi wanaumia, tabia ya kuzoea shida, matatizo na machozi ya watu hatuwezi kuivumilia.”

“Jambo limekaa miaka mitano mnataka likae miaka mingapi, upuuzi huu sitaki kusikiliza mnalipa lini? Jumatano ijayo mkae mtoke na majibu, tafuteni mtakachouza muwalipe watu pesa zao,” amesisitiza.

Wakati huohuo, Waziri Mkuu amekagua mradi wa ujenzi wa hospitali ya Halmashauri ya Manispaa ya Moshi inayojengwa katika Kata ya Ng’ambo kwenye manispaa hiyo.

Mradi huo ambao hadi kukamilika kwake unatarajiwa kugharimu sh. bilioni 6.59, hadi sasa ujenzi wake umefikia asilimia 55 ya katika majengo ya huduma za wagonjwa wa nje, huduma za mama na mtoto kwa miundombinu ya sakafu ya chini na ya kwanza.



Kupitia Programu ya Uwekezaji kwa Jamii, Benki ya NMB imekabidhi misaada ya madawati 100, viti 100 na meza 100 kwa shule mbili za msingi na moja ya sekondari wilayani Malinyi, mkoani Morogoro, vyote vikiwa na thamani ya Sh. Mil. 21.6.

Msaada huo ni sehemu ya Sh. Bil. 7.4 zilizotengwa na benki hiyo kwa ajili ya kusaidia miradi ya kijamii katika Sektra za Elimu, Afya na Mazingira kwa mwaka 2026, ikiwa ni asilimia moja ya Faida Baada ya Kodi ya Mwaka wa Fedha ulioishia Desemba 31, 2025.

Meneja wa NMB, Kanda ya Kati, Bi. Janeth Shango, ndiye aliyekabidhi misaada hiyo kwa Mkuu wa Wilaya ya Malinyi, Mhe. Sebastian Waryuba, aliyeipokea kwa niaba ya walimu wakuu wa Shule za Msingi Madibila Chini, Salamiti na Shule ya Sekondari Kilosa Mpepo, zote za Malinyi.

Akizungumza katika hafla iliyofanyika shule ya sekondari Kilosa Mpepo, Bi. Shango alisema Shule ya Madibila Chini imepewa madawati 50, idadi sawa na waliyopewa Shule ya Msingi Salamiti, huku Shule ya Sekondari ya Kilosa Mpepo ikisaidiwa viti 100 na meza 100 kwa ajili ya wanafunzi.

Msaada huu ni uthibitisho wa ushiriki wa Benki ya NMB katika maendeleo ya kijamii na kurejesha kwa jamii kutokana na faida walioipata. Na ni kupitia michango hii, Benki ya NMB imeweza kusaidia katika mbadiliko kwenye sekta ya elimu na pia kuifanya kutwa tuzo ya Benki Kinara wa Uwajibikaji kwa Jamii kutoka Jarida la Global Banking and Magazine la Marekani.

Kwa upande wake, DC Waryuba, aliishukuru na Kuipongeza Benki ya NMB kwa msaada huu wenye thamani ya Sh. Mil. 21.6. huku akibainisha kuwa kwa hesabu za haraka haraka utagundua kuwa kupitia madawati, viti na meza hizi, zinaenda kuwatoa sakafuni watoto takribani 500 wa shule hizi waliokuwa wakisoma chini.

DC Waryuba aliongeza kuwa tayari NMB imefungua njia katika kuboresha elimu wilayani Malinyi na kuwataka wadau zaidi kufuata nyayo za benki hiyo kwa kujitolea kusaidia, huku akiwasisitiza walimu na wanafunzi umuhimu wa kutunza misaada hiyo ili kuwatia moyo wafadhili hao.


Mkuu wa Wilaya ya Malinyi, Sebastian Waryuba akionyesha ishara ya shukrani baada ya benki ya NMB kukabidhi vifaa vya shule kwa wilaya hiyo vyenye thamani ya sh21.6milioni katika hafla iliyofanyika shule ya sekondari ya Kilosampepo mkoa wa Morogoro, wa pili kutoka kulia ni Meneja wa benki ya NMB kanda ya kati, Janeth Shango na wengine ni wanafunzi wa shule hiyo.


Mkuu wa Wilaya ya Malinyi, Sebastian Waryuba (aliyekaa) akifurahia jambo na Meneja wa benki ya NMB kanda ya kati, Janeth Shango pamoja na wanafunzi baada ya Benki hiyo kukabidhi vifaa vya shule vyenye thamani ya sh21.6milioni katika hafla iliyofanyika katika shule ya sekondari ya Kilosampepo mkoa wa Morogoro.

Mkuu wa Wilaya ya Malinyi, Sebastian Waryuba (wa tatu kushoto) akikabidhiwa mmoja ya meza 100 na Meneja wa benki ya NMB kanda ya kati, Janeth Shango (wa pili kulia) katika hafla ya benki hiyo ya kukabidhi vifaa vya shule wilaya ya Malinyi vyenye thamani ya sh21.6milioni iliyofanyika katika shule ya sekondari ya Kilosampepo mkoa wa Morogoro. Kulia ni meneja wa Benki ya NMB tawi la Malinyi, Anderson Lyatuu na kuhoto ni wawakilishi wa shule nufaika wa msaada huo.

Balozi wa Canada nchini, Mheshimiwa Emily Burns, akiangalia mashine ya teknolojia ya kisasa ya uchimbaji madini bila kulazimika kushuka chini ya ardhi alipotembelea mgodi wa Barrick Bulyanhulu.

Balozi wa Canada nchini , Mheshimiwa Emily Burns akiangalia moja ya vifaa vilivyo chini ya mgodi alipotembelea sehemu ya chini ya mgodi (underground) kwenye mgodi wa Barrick Bulyanhulu , wa kwanza kushoto ni Meneja Mkazi wa Barrick nchini, Dkt. Melkiory Ngido.

Balozi wa Canada nchini , Mheshimiwa Emily Burns (wa pili kutoka kulia) akiangalia shughuli za uzalishaji chini ya mgodi (Underground) kwenye ziara yake ya kikazi katika mgodi wa Barrick Bulyanhulu kulia ni Meneja Mkazi wa Barrick nchini, Meneja Mkazi wa Barrick nchini, Dkt. Melkiory Ngido.

Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Bugarama , Dkt. Beatha Alistides akibadilishana mawazo na Balozi wa Canada nchini , Mheshimiwa Emily Burns, alipotembelea hospitali hiyo ambayo imefadhiliwa na Mgodi wa Barrick Bulyanhulu.

Balozi wa Canada nchini, Mheshimiwa Emily Burns akitembezwa katika maeneo ya kituo cha afya cha Bugarama

Balozi wa Canada nchini, Mheshimiwa Emily Burns, akifuatilia wasilisho kuhusiana na shughuli za Barrick nchini alipofanya ziara ya kikazi katika mgodi wa Bulyanhulu.

Meneja Mkazi wa Barrick nchini, Dkt. Melkiory Ngido akiwa kwenye kikao kwenye ujio wa Balozi wa Canada nchini Mheshimiwa Emily Burns (hayupo Pichani) alipotembelea mgodi wa Barrick Bulyanhulu

Baadhi ya wafanyakazi wa Barrick wakati wa mkutano na Balozi wa Canada nchini , Mheshimiwa Emily Burns alipotembelea mgodi wa Bulyanhulu.


**
Balozi wa Canada nchini Tanzania Mhe. Emily Burns, amefanya ziara ya kikazi katika mgodi wa dhahabu wa Barrick Bulyanhulu uliopo katika halmashauri ya wilaya ya Msalala mkoani Shinyanga na kupongeza uendeshaji wa mgodi huo kwa viwango vya kimataifa sambamba na kufanikiwakutekeleza malengo Endelevu ya Dunia (SDGs) kwa vitendo.


Mhe. Burns, katika ziara hiyo ametembelea maeneo ya uzalishaji na kuona jinsi kampuni ya Barrick ilivyowekeza katika matumizi ya teknolojia za kisasa na zenye usalama kwa wafanyakazi katika shughuli za uchimbaji ambapo pia alitembelea baadhi ya miradi ya kijamii iliyotekelezwa kwa fedha za uwajibikaji kwa jamii kutoka mgodi wa Barrick Bulyanhulu ambayo ni kituo cha afya cha Bugarama na shule ya sekondari ya Bugarama.


Akiongea baada ya ziara hiyo Balozi Burns, ametoa pongezi kwa kampuni ya Barrick nchini kwa kuendesha migodi yake nchini kwa weledi mkubwa sambamba na kuhakikisha uwekezaji wake unaleta manufaa kwa jamii zinazozunguka maeneo ya migodi kupitia utekelezaji wa miradi ya kijamii na kutoa mchango wa ukuzaji uchumi wa taifa kwa ujumla kupitia kulipa kodi Serikali na kupanua wigo wa ajira kwa watanzania walioajiriwa migodini na wale wenye ajira zisizo za moja kwa moja ikiwemo wazabuni wanaofanya kazi na migodi.


"Nachukua nafasi hii kuipongeza kampuni ya Barrick kupitia Mgodi wake wa Barrick Bulyanhulu kwa jinsi unavyoendesha shughuli zake za uzalishaji kwa weledi kwa kuzingatia Usalama kwa Wafanyakazi wake na kwa jinsi unavyoshirikiana na Serikali na Jamii inayozunguka mgodi kwa kuwawezesha miradi ya maendeleo pamoja na vikundi mbalimbali vya wajasiriamali",amesema Balozi Emily Burns.


Naye Meneja Mkazi wa Barrick nchini, Dkt. Melkiory Ngido, ametoa shukrani kwa Balozi wa Canada nchini kwa kutembelea mgodi wa Barrick Bulyanhulu na kutembelea baadhi ya miradi ya kijamii iliyotekelezwa na mgodi huo ambayo imelenga kuboresha maisha ya wananchi wanaoishi maeneo ya jirani na mgodi na jamii kwa ujumla.


"Kwetu ziara hii ni chachu ya kujifunza na kupokea maoni kutoka kwa wadau ili kuongeza jitihada za kufanya vizuri zaidi",amesema.


Dkt. Ngido ameongeza kuwa dhamira ya kampuni ya Barrick inayoendesha shughuli zake nchini kwa ubia na Serikali kupitia kampuni ya Twiga Minerals ni kuunga mkono jitihada za serikali kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na mahitaji muhimu ili kunufaika na uwekezaji wake nchini.


Aidha ameongeza kuwa utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kijamii ni mkakati endelevu wa kampuni ya Barrick unaojumuisha ushirikiano na wadau na vipaumbele ambavyo vimelenga kufanikisha kuleta mabadiliko chanya kwenye jamii zinazoishi kwenye maeneo yaliyopo Jirani na migodi yake sambamba na kufanikisha utekelezaji wa Malengo Endelevu ya Dunia (SDGs).
NA EMMANUEL MBATILO, MICHUZI TV

WAKALA wa Vipimo (WMA) wameendelea kuendelea kutoa elimu kwa wafanyabiashara kuhusu matumizi sahihi ya mizani na vipimo badala ya kutumia nguvu katika utekelezaji wa sheria kwa wale ambao wanakaidi agizo.

Akizungumza katika kikao na wafanyabiashara wa masoko leo jijini Dar es Salaam Meneja wa WMA Mkoa wa Ilala, Muhono Nashon amesema lengo la elimu hiyo ni kujenga uelewa wa pamoja kabla ya maafisa wa vipimo kuanza ukaguzi mitaani.

Amefafanua kuwa wakala umejikita katika kutoa mafunzo kwa wafanyabiashara wanaotumia mizani ya aina mbalimbali ili kuhakikisha wanazingatia viwango vinavyotakiwa kisheria.

“Tunataka tunapokwenda kufanya ukaguzi tuwe tunaongea lugha moja na wafanyabiashara. Elimu ni muhimu kwa sababu wapo wapya sokoni na wengine hawafahamu taratibu za vipimo,” amesema Nashon.

Nashon aliongeza kuwa utoaji wa elimu ni endelevu, hasa katika mazingira ya masoko yanayopokea wafanyabiashara wapya mara kwa mara. Alisema baadhi ya changamoto hutokana na kutofahamu sheria, huku wengine wakifanya makosa kwa makusudi ili kujinufaisha.

Kwa upande wake, Katibu Msaidizi wa Soko la Ilala, Juma Bakari, aliiomba serikali kuhakikisha kunakuwa na usawa katika utekelezaji wa sheria za vipimo kuanzia mashambani hadi masokoni.

“Ni muhimu elimu hii ikaenda hadi kwa wakulima mashambani. Pia vyombo vya habari vitumike kuelimisha umma ili kila mtu afahamu viwango vinavyotakiwa,” amesema Bakari.

Bakari amesisitiza kuwa utekelezaji usio sawa unaweza kuibua malalamiko ya upendeleo au vitendo vya rushwa.

Nao baadhi ya wafanyabiashara wa jumla wameeleza changamoto wanazokutana nazo wanaposafirisha mazao kutoka mikoa mbalimbali kwenda Dar es Salaam. Walisema mara kadhaa hulipa faini njiani na wanapofika sokoni hukumbana tena na adhabu kwa madai ya kuzidisha ujazo wa magunia.

Mfanyabiashara wa viazi, Stella Mwakamboje, alisema tofauti ya vifungashio kama “mfuto” au “rumbesa” katika mikoa ya Mbeya na Njombe huleta mkanganyiko wa bei na ushindani usio sawa sokoni.

Amesema hali hiyo huathiri uwezo wa wafanyabiashara kurejesha mikopo wanayochukua kuendesha biashara.

Wafanyabiashara hao wameiomba serikali kuweka utaratibu mmoja wa kitaifa wa vifungashio na vipimo ili kuondoa tofauti hizo.

Wamesisitiza kuwa iwapo mizani itatumika rasmi, basi iwe kwa wote kuanzia mashambani hadi masokoni ili kuleta usawa wa kibiashara.

Mwenyekiti wa Soko la Ilala, Ali Mbiku, ameipongeza WMA kwa kutoa elimu hiyo, akisema itasaidia kulinda maslahi ya walaji na wafanyabiashara.

“Matumizi ya mizani yatasaidia mfanyabiashara kujua faida halisi badala ya kutegemea makadirio ya ujazo wa gunia,” amesema Mbiku.

Sambamba na hayo, Mbiku amelalamikia baadhi ya halmashauri kutoza faini kwa madai ya ukiukwaji wa vipimo wakati mamlaka ya kusimamia vipimo ipo kwa Wakala wa Vipimo pekee. Alisema ni muhimu mamlaka husika zishirikiane ili kuondoa migongano inayowaumiza wafanyabiashara.





















Dar es Salaam, Februari 20, 2026 
KAMPUNI ya Airtel Tanzania imemkabidhi gari jipya aina ya Mazda CX-5 Bw. Shakuu Joshua, dereva taxi mwenye umri wa miaka 31 kutoka Kimara-Temboni, baada ya kuibuka mshindi wa zawadi kuu katika kampeni inayoendelea ya “Mwaka Umenyooka na My Airtel Money App.”

Bwana Joshua ameshinda gari mpya baada ya kununua luku ya umeme yenye thamani ya TZS 1,000 kupitia My Airtel Money App. Baada ya kukamilisha muamala huo, alishiriki katika kipengele cha mchezo wa kusokota (digital spin) ndani ya programu hiyo na baadaye kuthibitishwa kuwa mshindi wa zawadi ya juu kufuatia mchakato rasmi wa uhakiki wa Airtel.

Gari hilo limekabidhiwa rasmi nyumbani kwa familia yake huko Ubungo-Msewe, Dar es Salaam, mbele ya wanafamilia na wawakilishi wa jamii.

Akizungumza wakati wa sherehe za makabidhiano, Bwana Joshua amesema taarifa za ushindi huo awali zilikuja kama mshangao. “Kushinda hii Mazda CX-5 imekuwa mshtuko mkubwa. Uzoefu huu umebadilisha maisha yangu kikweli.

 Ninaishukuru sana Airtel kwa fursa hii. Mke wangu amepata mtoto hivi karibuni, hivyo gari hili halitasaidia tu mahitaji ya familia yangu bali pia litafungua fursa mpya kwa kazi yangu na maisha ya baadaye. Hii ni hatua kubwa, na ninahisi nimehamasika kufikia makubwa zaidi nikijua kuwa hatua ndogo kama kutumia Airtel Money, inaweza kuleta zawadi kubwa,” amesema Bwana Shakuu Joshua.

Mama wa mshindi wa gari, Bi. Magreth Mtei, ameelezea shukrani na furaha yake kufuatia makabidhiano hayo.

“Namshukuru Mungu! Nina furaha sana na nimejawa na shukrani. Nilipoambiwa kuwa mwanangu ameshinda kupitia Airtel, kwa kweli kwa mda huo sikuweza kuamini. Nilipoliona gari lenyewe kwa macho yangu leo, ndo nikasema kweli mwanangu ameshinda gari. Naishukuru sana Airtel kwa kuwapa watoto wetu na familia fursa nzuri kama hii,” amesema.

Kwa mujibu wa Airtel Tanzania, kampeni hiyo inawahimiza wateja kufanya miamala kupitia My Airtel Money App, ikiwa ni pamoja na kutuma na kupokea pesa, kulipia bili, kununua muda wa maongezi na kununua luku. Miamala inayokidhi vigezo huingiza wateja moja kwa moja kwenye droo za kampeni na mifumo ya kidijitali ya kutoa zawadi.

Mkurugenzi wa Airtel Money, Andrew Lugamba, amebainisha kuwa kampeni hiyo inaendelea kurekodi ushiriki mkubwa nchi nzima.

“Hadi sasa, kampeni imetoa zaidi ya Bajaj saba, seti za televisheni zaidi ya 30, pikipiki nane, na gari moja la Mazda CX-5. Magari mengine mawili ya Mazda CX-5 yamepangwa kutolewa kabla ya kampeni kuhitimishwa. Lengo letu ni kutoa zawadi kwa uaminifu wa wateja wetu huku tukiimarisha ujumuishaji wa huduma za kifedha kidijitali,” amesema. Airtel Tanzania imesisitiza dhamira yake ya kupanua ufikiaji wa huduma za kifedha za kidijitali zilizo rahisi na salama kupitia kampeni zinazomlenga mteja na mifumo inayochochewa na teknolojia.

Watuhumiwa saba wamefikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Same leo, Februari 19, 2026, wakikabiliwa na mashtaka mbalimbali yanayohusiana na dawa za kulevya aina ya mirungi, huku mmoja wao akiwekewa amri ya kuwa chini ya uangalizi wa Polisi kwa miaka mitatu.

Kwa mujibu wa taarifa za mahakama, kesi saba zimefunguliwa, kila moja ikiwa na mtuhumiwa mmoja. Watuhumiwa wote walisomewa mashtaka yao na walikana tuhuma zinazowakabili, na mashauri yao kupangiwa tarehe nyingine.

Katika kesi ya kwanza, Goodlak Bariki Mungulu anashtakiwa kwa kupatikana na mirungi yenye uzito wa kilo 1.8. Shtaka hilo liliwasilishwa na Wakili wa Serikali, Jackson Matowo, mbele ya Mheshimiwa Christanta Chitanda, Hakimu Mfawidhi. Mshtakiwa alikana shtaka hilo na shauri lake limepangwa kutajwa tena Juni 24, 2024. Ingawa shauri hilo lina dhamana, mshtakiwa ameshindwa kutimiza masharti ya dhamana.

Kesi ya pili inamhusu Athuman Tuarira Kivuma, anayekabiliwa na shtaka la kusafirisha mirungi yenye uzito wa kilo 27. Shtaka liliwasilishwa na Wakili Matowo mbele ya Hakimu Chitanda. Mshtakiwa alikana na shauri lake limepangwa tena Juni 24, 2024.

Katika kesi ya tatu, Nuru Mbonea Mndeme anashtakiwa kwa kusafirisha mirungi kilo 25. Mashtaka yake yalisomwa mbele ya Hakimu Chitanda, naye alikana. Shauri lake limepangwa tena Februari 24, 2026.

Kesi tatu nyingine zilisikilizwa mbele ya Mheshimiwa Hellen Hozza, Hakimu Mkazi Mwandamizi. Katika mashauri hayo, Youze Eliwaha Kitua anakabiliwa na shtaka la kusafirisha mirungi kilo 34, Ahadi Mbazi Mnjama kilo 26 na Edson Elihazina Kibaja kilo 24. Mashtaka yao yalisomwa na Wakili wa Serikali Alex Rusibamayila, na wote walikana tuhuma hizo. Mashauri yao yamepangwa tena Machi 2, 2026; Machi 4, 2025; na Machi 3, 2026 mtawalia.

Kwa upande wa kesi ya saba, Mganga Wahidi Dorovu alipandishwa mahakamani kwa ajili ya kuwekewa chini ya uangalizi ya kuwa na tabia njema ya kutokufanya uhalifu wowote. Mahakama iliamuru awe chini ya uangalizi wa Polisi Same kwa kipindi cha miaka mitatu na kuripoti kituoni kila mwezi, kwa masharti ya kutojihusisha na uhalifu wowote, ikiwemo biashara au matumizi ya dawa za kulevya.

Hatua hiyo inaonyesha kuendelea kwa juhudi za vyombo vya dola katika kukabiliana na biashara na usafirishaji wa dawa za kulevya katika Wilaya ya Same na maeneo jirani.




Top News