Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa, Mohamed Ahmed akizungumza jijini Dar es Salaam Machi 13, 2026 katika hafla ya futari kwa Waislam na Wakristu iliyoandaliwa na TCD kwa wadau wa demokrasia na vyama vya siasa.


Na Mwandishi Wetu.
KITUO cha Demokrasia Tanzania (TCD) kimeendelea kuimarisha juhudi za kuvikutanisha vyama vya siasa nchini kwa lengo la kujadili masuala mbalimbali ya kitaifa na kukuza utamaduni wa majadiliano unaochochea demokrasia, amani na mshikamano wa kitaifa.

Akizungumza jijini Dar es Salaam Machi 13, 2026 katika hafla ya futari kwa Waislam na Wakristu iliyoandaliwa na TCD kwa wadau wa demokrasia na vyama vya siasa, Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa, Mohamed Ahmed, alisema majadiliano ya wazi na vikao vya pamoja kati ya vyama vya siasa ni muhimu katika kujenga demokrasia imara na kuimarisha utulivu wa nchi.

Alisema Tanzania imeendelea kujitofautisha na mataifa mengine kwa kudumisha amani na utulivu, akibainisha kuwa misingi hiyo inalindwa na utamaduni wa kuvumiliana na kushirikiana licha ya tofauti za kisiasa.

“Watanzania tunapaswa kuendelea kulinda amani yetu kwa kutumia majukwaa ya mazungumzo na maridhiano. Njia zinazoweza kuhatarisha utulivu wa nchi hazina nafasi katika jamii yetu,” alisema Ahmed.

Awali, Mwenyekiti wa TCD, Dorothy Semu, alisema taasisi hiyo ina jukumu la kuvikutanisha vyama vya siasa ili kujadiliana masuala muhimu ya kisiasa na kitaifa licha ya tofauti za kiitikadi na kimtazamo.

Alisema mfumo wa vyama vingi unatoa nafasi ya kushindanisha mawazo na sera mbalimbali kwa lengo la kupata suluhisho bora kwa maendeleo ya taifa, huku akisisitiza kuwa tofauti za kisiasa hazipaswi kutafsiriwa kama uadui bali fursa ya kujifunza na kuboresha mifumo ya uongozi.

Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF) Tanzania Bara, Miraj Mtibwiriko, alisema pamoja na kuwepo kwa vyama vingi na mitazamo tofauti ya kisiasa, ni muhimu kwa Watanzania kuendelea kudumisha umoja wa kitaifa kwa kuwa lengo la vyama vyote ni kuboresha maisha ya wananchi.

Naye Katibu Mkuu wa Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMA), Salum Mwalimu, alisema chama hicho kimejiunga na TCD baada ya uchaguzi wa mwaka 2025 na kimejipanga kushirikiana kikamilifu katika kukuza demokrasia nchini.

Alisema TCD imekuwa jukwaa muhimu la kuimarisha mazungumzo ya kisiasa na kutoa elimu kwa vyama vya siasa kupitia makongamano, semina na mafunzo mbalimbali.

TCD ni taasisi inayovikutanisha vyama vya siasa vyenye uwakilishi bungeni, katika mabaraza ya madiwani na Baraza la Wawakilishi kwa lengo la kukuza demokrasia, haki na amani nchini kupitia majadiliano na ushirikiano wa wadau wa kisiasa.




Matukio mbalimbali katika picha.

📌Miundombinu mipya imerahisisha usafirishaji wa vikonyo vya mimea na kuchochea maendeleo Arumeru

Arumeru, Arusha

Wananchi wa kijiji cha Duluti wilayani Arumeru mkoani Arusha wameweka mkakati wa kupanda miti kandokando ya barabara mpya ya lami ya Sangisi-Nambala yenye urefu wa Km 4.2 iliyojengwa katika eneo hilo ili kulinda miundombinu dhidi ya mmomonyoko wa ardhi na kuhakikisha inadumu kwa muda mrefu.

Hatua hiyo imekuja baada ya wananchi kunufaika na ujenzi wa barabara hiyo iliyojengwa na Serikali kupitia Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) ambapo kipande cha Km. 2.36 kimekamilika 

Akizungumza kuhusu mpango huo, Mwenyekiti wa kijiji cha Duluti Bw. Harisi Kaaya, amesema wananchi wameamua kuchukua jukumu la kulinda barabara hiyo kwa kupanda miti katika maeneo maalum kandokando ya barabara kwani  kwa miaka mingi ilikua katika hali mbaya na kusababisha adha kubwa kwa wakazi wa eneo hilo.

Amesema kabla ya kuanza utekelezaji wa mpango huo, wananchi walifanya kikao na mkandarasi wa mradi huo ili kupata ushauri wa kitaalamu kuhusu umbali unaofaa wa kupanda miti bila kuathiri miundombinu ya barabara.

“Tumekaa kikao na kumuomba mkandarasi atuoneshe umbali sahihi wa kupanda miti ili kuilinda barabara hii. Sisi wananchi tuna dhamira kubwa ya kuitunza kwa sababu tumekaa miaka mingi sana bila kuwa na barabara ya lami na tumeteseka kwa muda mrefu,” amesema Kaaya.

Ameeleza kuwa tangu wakiwa watoto hawakuwahi kushuhudia barabara ya lami katika eneo hilo, kwani kwa muda mrefu barabara hiyo ilikuwa ikitumika zaidi kupitisha mazao ya kahawa pamoja na mazao mengine ya kilimo kutoka maeneo ya chini kwenda sokoni.

Ameongeza kusema kwamba wakati wa mvua barabara hiyo ilikuwa haipitiki kabisa kutokana na mmomonyoko wa ardhi na maji ya mvua yaliyokuwa yakiharibu miundombinu hiyo.

“Tunamshukuru Mungu na serikali kwa sasa kuwa na barabara ya kiwango cha lami. Zamani wakati wa masika barabara ilikuwa haipitiki kabisa kutokana na maporomoko ya mvua na uharibifu wa barabara,” amesema.

Kaaya ameongeza kuwa ujenzi wa barabara hiyo umeleta nafuu kubwa kwa wananchi kwa kupunguza gharama za usafiri na kurahisisha usafirishaji wa mazao kwenda katika Soko la Tengeru.

“Kwa kweli tuna furaha sana. Hapo awali tulikuwa tunalipa nauli ya shilingi 2,000 kufika Tengeru, lakini kwa sasa tunalipa takribani shilingi 500 kwa kutumia bajaji. Hii imerahisisha maisha ya wananchi na kuongeza fursa za biashara,” amesema.

Kwa upande wake, Meneja wa kampuni inayojihusisha na usafirishaji wa vikonyo vya maua katika eneo hilo Bw. Nelson Shilinde, amesema ujenzi wa barabara ya lami ya Malalua-Nduruma-Bwawani Km. 28 ambapo kwasasa kipande cha mita 650 kimekamilika umekuwa na manufaa makubwa kwa shughuli zao za kilimo.

Amesema hapo awali vumbi lililotokana na ubovu wa barabara lilikuwa linaathiri mimea yao, kwani vumbi lilikuwa linaganda kwenye plastiki za ‘greenhouses’ na kuzuia mwanga wa jua kupenya ipasavyo.

“Mimea yetu inahitaji mwanga wa kutosha wa jua ili kustawi. Zamani vumbi lilikuwa linaganda kwenye plastiki  na kuathiri ukuaji wa mimea. Lakini sasa hali hiyo haipo kutokana na ujenzi wa barabara ya lami,” amesema.

Amesema pia usafirishaji wa miche na mazao yao umeboreshwa kwa kiasi kikubwa, kwani magari yao sasa yanapita kwa urahisi bila kuharibika mara kwa mara kama ilivyokuwa awali.









Na Mwandishi Wetu,Kilimanjaro

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dkt.Samia Suluhu Hassan ametoa  Shilingi Bilioni 25 ikiwa ni utekelezaji wa ahadi aliyoitoa wakati wa Kikao cha Maafisa Wakuu Waandamizi wa Jeshi la Polisi kilichofanyika mwaka 2024 lengo ikiwa kuifanyia maboresho Shule cha Polisi Kilimanjaro ambacho kinakabiliwa na uchakavu wa Majengo ambayo yalijengwa tangu  mwaka 1933 ambapo yanajumuisha Mabweni ya Wanafunzi,Madarasa na Nyumba za Askari.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,Patrobas Katambi wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje Ulinzi na Usalama(NUU) iliyotembelea shule hiyo kukagua matumizi ya fedha hiyo iliyotolewa na Mheshimiwa Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan ikiwa ni utaratibu wa Kamati za Bunge kufuatilia matumizi ya fedha zinazotolewa na serikali kwa miradi mbalimbali ya maendeleo.

“Leo tunazungumza Wizara ya Mambo ya Ndani ambapo Rais ameweza kuyafanya haya ambayo wajumbe mmeyashuhudia leo kwa kiasi cha Shilingi Bilioni 25 ambazo mmeona kwa kiwango kikubwa na uweledi mkubwa wa jeshi katika utekelezaji na uwezo wa kusimamia kazi.Kwa kweli hatuna namna ya kuweza kumshukuru Mheshimiwa Rais Zaidi ya kumuombea afya njema,umri na rizki ili Mwenyenzi Mungu aendelee kumpa hekima na busara ili sisi wizara tuendelee kuwa wanufaika wa uongozi wake” amesema Waziri Katambi

“Lakini tuna miradi ya ujenzi wa nyumba sehemu mbalimbali ambapo Mheshimiwa Rais pia anatoa kiasi kikubwa cha fedha na pale Dodoma tayari mradi ushaanza na tunatumia wataalamu wetu wa ndani na wanajenga kwa viwango vile vile kama mlivyoona hapa Shule ya Polisi,tunaenda kufanya maboresho ya maslahi kwa askari,mabadiliko ya sera na sheria  na teknolojia za kisasa pia zinaendelea kuingizwa jeshini ili vifaa vya kisasa vitumike katika kulinda usalama wetu.”Aliongeza Waziri Katambi

Akizungumza katika ziara hiyo,Mwenyekiti wa Kamati hiyo ya NUU, Najma Murtaza Giga, ametoa pongezi kwa Jeshi la Polisi kwa kujenga mradi huo kwa ufanisi na uweledi mkubwa huku akikiri kuona thamani ya kiasi cha fedha kilichotolewa na Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan huku akiweka wazi Kamati kuendelea  kuwa na imani na Jeshi la Polisi katika masuala mbalimbali na hivyo haina budi kuendelea kulisemea Jeshi la Polisi kuhakikisha linawezeshwa ili liweze kutekeleza majukumu yake ya kulinda usalama wa raia na mali zao kwa weledi na ufanisi wa hali ya juu.

Nae Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Camillus Wambura, ameishukuru Kamati hiyo ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) kwa kutenga muda na kuona umuhimu wa kutembelea Shule ya Polisi Tanzania-Moshi mkoani Kilimanjaro na kuona thamani ya fedha iliyotolewa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, inavyotumika kwa kuhakikisha ubora na ufanisi unaonekana kwenye miradi hiyo ya ujenzi.

Aidha, IGP Wambura, ameiambia kamati hiyo kuwa, serikali ya awamu ya sita imeendelea kuliwezesha Jeshi la Polisi kwenye miundombinu mbalimbali kote nchini ili kuhakikisha askari Polisi wanafanya kazi kwenye mazingira mazuri na wezeshi katika kuwahudumia wananchi, kutatua kero mbalimbali ili waendelee kufanya kazi zao bila uwepo wa matishio ya kihalifu nchini.









Na: Dk. Reubeni Lumbagala, Tanga

Maji ni kimiminika muhimu kwa maisha na uhai wa viumbei. Maji hutumika kuanzia asubuhi, mchana, jioni hadi usiku. Hutumika kwa matumizi ya nyumbani kama kupikia, kufulia na kuogea. Hutumika katika shughuli za kiuchumi kama viwandani, mashambani, migodini, masokoni kutaja kwa uchache. Maji hayana mbadala, panapohitajika maji, hakuna namna nyingine bali kuyatafuta na kukidhi haja yake. Hakuna siku inaweka kupitia bila kutumia maji. Maji ni uhai na maji ni maisha. Binadamu anahitaji maji kila siku. 

Tanzania imebarikiwa kuwa na vyanzo vingi vya maji. Mathalani; bahari, maziwa, mito, mabonde. Vyanzo hivi husaidia kupata maji kwa matumizi mbalimbali. Kutokana na ongezeko kubwa la watu nchini na shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi, mahitaji ya huduma ya maji pia yameongezeka sana.

 Wizara ya Maji yenye dhamana ya usambazaji wa huduma ya maji katika maneno mbalimbali nchini ina wajibu mkubwa wa kuhakikisha maji yanawafikia wahitaji ili kuchochea shughuli mbalimbali za kimaendeleo nchini.

Rais Dk. Samia Suluhu Hassan ni mdau mkubwa wa sekta ya maji. Anatambua umuhimu wa maji kwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi. Kutokana na hilo, amekuwa akiongeza fedha katika bajeti ya Wizara ya Maji kila mwaka, jambo linalosaidia utekelezaji wa miradi ya maji ambayo inakwenda kutatua changamoto za maji katika maeneo mbalimbali nchini na kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwani maji ni kiungo muhimu sana. 

Mathalani kwa mwaka wa fedha 2025/2026, Bajeti ya Wizara ya Maji ilikuwa Sh. 1.01 trilioni ambapo katika fedha hizo, Sh. 943.22 bilioni zilikuwa ni kwa ajili ya miradi ya maendeleo. Hii inaonyesha namna Wizara ya Maji ilivyojizatiti kutatua kero za wananchi kwa kupeleka fedha nyingi kwenda kwenye miradi ya maji.

Rais Dk. Samia pia ameelekeza Wizara ya Maji kufanikisha mradi kabambe wa Gridi ya Taifa ya Maji kama ilivyo Gridi ya Taifa ya Umeme inayosimamiwa na Wizara ya Nishati ili kuhakikisha nchi inakuwa na uhakika wa maji kwa shughuli mbalimbali za maendeleo. Kwa nchi yetu yenye utajiri wa vyanzo vya maji, mradi wa Gridi ya Taifa ya Maji ni suala muhimu hasa kipindi hiki ambacho dunia inapitia changamoto ya mabadiliko ya tabia ya nchi. 

Gridi ya Taifa ya Maji itakusanya maji kutoka vyanzo mbalimbali vya maji nchini kwa matumizi ya kimaendeleo. Kilimo ambacho ndiyo uti wa mgongo wa uchumi wetu kinahitaji sana raslimalimaji kwa ajili ya umwagiliaji. Kilimo cha kutegemea maji ya mvua pekee hakitoi uhakika kwa kupata mavuno kwani endapo kutatokea ukame au uhaba wa mvua, mazao yatanyauka na kufa kabisa.

 Uwepo wa maji ya kutosha unatoa uhakika wa kuvuna, kupata chakula na fedha baada ya kuuza mazao ndani na nje ya nchi. Maji yanawezesha pia uzalishaji wa umeme wa nguvu za maji (Hydo-Electric Power - HEP).

Maji ya uhakika yanatoa uhakika wa uendelevu wa shughuli za ufugaji. Wanyama na ndege watapata maji ya kunywa na majosho ya kuogeshea wanyama. Uvuvi unategemea uwepo wa maji, ukosefu wa maji unarudisha nyuma shughuli za uvuvi ambazo ni muhimu kwa uchumi wetu. Maeneo ya biashara kama masokoni vilevile wanahitaji maji kwa ufanisi wa shughuli zao. Wachimbaji wa madini na wahandisi wa ujenzi nao wanahitaji maji katika shughuli zao. Maeneo ya taasisi kama shule na hospitali, nao bila maji maisha hayaendi.

Katika kufanyia kazi maelekezo ya Rais Dk. Samia kuhusiana na mradi wa Gridi ya Taifa ya Maji, hivi karibuni Waziri wa Maji Jumaa Aweso, Katibu Mkuu Wizara ya Maji Mhandisi Mwajuma Waziri pamoja na watendaji wa sekta ya Maji walifanya ziara katika Jimbo la Shan Dong Kaskazini mwa China kuona na kujifunza namna walivyofanikiwa kuviunganisha vyanzo vya mito na maziwa katika Gridi ya Taifa ya Maji kutoka Kaskazini hadi Kusini mwa China.

Kimsingi, mpango uliopo nchini ni kuviunganisha vyanzo mbalimbali vya maji nchini kama vile Maziwa ya Viktoria, Tanganyika na Nyasa pamoja na mito ya Rufiji, Kagera, Kiwira, Wami, Pangani, Ruvu na Ruvuma na vyanzo vingine ili kuwa na uhakika wa maji kwa maendeleo ya sekta mbalimbali. 

Katika kutekelekeza miradi huu, ni vyema wananchi tukawa mabalozi wazuri wa kutunza vyanzo vya maji vilivyopo na kutunza mazingira kwa ujumla. Tukumbuke maji hayana mbadala, kila mtu anahitaji maji. Kwa hakika, mafanikio ya kuwa na Gridi ya Taifa ya Maji ni uhakika wa kupata maendeleo endelevu. Tuunge mkono mradi huu muhimu kwa manufaa ya kizazi cha leo na kijacho. Tafakari.

Maoni: 0620 800462.








WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, ameweka jiwe la msingi la mradi wa ujenzi wa barabara ya Kagwira – Karema (kilometa 112) katika Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika mkoani Katavi.

Mradi huo unatekelezwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) kwa gharama ya takribani shilingi bilioni 219.09, ukiwa na lengo la kuboresha miundombinu ya usafiri na kuchochea shughuli za kiuchumi katika ukanda wa Ziwa Tanganyika.

Kwa mujibu wa taarifa ya mradi iliyosomwa na Kaimu Meneja wa Udhibiti wa Miradi TANROADS, Mhandisi Malima Musema Mongo, ujenzi wa barabara hiyo umegawanyika katika vipande viwili ambavyo ni Kagwira – Kasekese (kilometa 54.144) na Kasekese – Ikola – Karema (kilometa 56.911).

Alisema ujenzi wa kipande cha Kagwira – Kasekese unagharimu takribani shilingi bilioni 106.95 na umefikia asilimia 8.2 ya utekelezaji, huku kipande cha Kasekese – Ikola – Karema kikigharimu takribani shilingi bilioni 112.14 na kufikia asilimia 33.4 ya utekelezaji.

Mradi huo ni wa kimkakati kwa kuwa utarahisisha usafirishaji wa mizigo kupitia Bandari ya Karema kwenda nchi jirani ikiwemo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, pamoja na kupunguza msongamano wa malori ya mizigo katika eneo la Tunduma.

Aidha, barabara hiyo itarahisisha usafirishaji wa mazao kutoka mashambani na kuwaunganisha wananchi na huduma mbalimbali za kijamii kama vile huduma za afya na biashara katika maeneo ya ukanda huo.

Mradi huo unatekelezwa kwa mfumo wa kimkataba na unatarajiwa kukamilika ndani ya kipindi cha miezi 26. Hadi sasa utekelezaji wa jumla wa mradi umefikia asilimia 21, ambapo kiasi cha shilingi bilioni 32.37 kimeshapokelewa na kutumika katika hatua mbalimbali za ujenzi.

Kukamilika kwa mradi wa barabara ya Kagwira – Karema kunatarajiwa kuwa kichocheo muhimu cha maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika Mkoa wa Katavi na maeneo jirani kwa kuimarisha usafiri, biashara na mawasiliano katika ukanda wa Ziwa Tanganyika.








Kamati ya kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii imempongeza Afisa Uhifadhi Mkuu wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro Dkt. Agnes Gidna kutokana na umahiri, umakini, kujiamini na uchambuzi wake mkubwa wa masuala ya mambo kale na jiolojia.

Wakiongozwa na mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Timotheo Mnzava wabunge hao wametoa pongezi hizo baada ya kukagua na kupata maelezo ya mradi wa makumbusho ya Urithi Geopark Museum. 

Wabunge wamepongeza kazi kubwa iliyofanywa na serikali ya Tanzania na China ambapo hawakusita kuelezea hisia zao kutokana na mtaalam huyo  alivyowakonga nyoyo kwa kuelezea historia kuhusa kutokea kwa kreta ya Ngorongoro, milpuko ya volkano, maumbile ya dunia, chanzo cha binadamu wa kale na masuala mengine.

Kamati ya Bunge imeielekeza wizara ya Maliasili na Utalii kuitumia makumbusho hiyo kama bidhaa ya utalii na kitovu cha elimu kwa vijana wa kitanzania na kimataifa.

Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt.Ashatu Kijaji aliwashukuru wabunge kwa pongezi hizo na kuwahakikishia kuwa wizara yake itasimamia kwa karibu maendeleo ya Urithi Geopark Museum.

Dkt.Agnes Gidna, mtaalam wa makumbusho, mambo kale na urithi wa utamaduni amekuwa kiungo muhimu  katika makumbusho hayo kutokana na umahiri wake wa kitaaluma na kitaalam kuihadithia yaliyopo kwenye makumbusho hiyo.







Na Mwandishi Wetu, Mbeya

MKUU wa Wilaya ya Mbeya, Solomon Itunda, amewahimiza viongozi wa dini ya Kiislamu kuendelea kusimamia na kuimarisha maadili kwa waumini hata baada ya kumalizika kwa mwezi mtukufu wa Ramadhan.

Itunda ametoa wito huo wakati wa hafla ya Iftari iliyoandaliwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, Erica Yegella, iliyolenga kuimarisha mshikamano miongoni mwa waumini, watumishi wa umma na wadau wa maendeleo.

Akizungumza katika hafla hiyo, Itunda amesema maadili yanayojengwa wakati wa Ramadhan yanapaswa kudumishwa katika maisha ya kila siku ili kulinda amani na utulivu wa nchi.

“Niwaombe viongozi wa dini kuendelea kuhamasisha waumini kutenda mema hata baada ya Ramadhan kupita. Kama viongozi wa umma, tunalo jukumu la kuendeleza uadilifu na kuwahudumia wananchi kwa haki,” amesema Itunda.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa amani akieleza kuwa ndiyo nguzo inayowezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo, ukiwemo upanuzi wa barabara kutoka Igawilo hadi Tunduma unaolenga kuimarisha miundombinu ya usafirishaji na biashara.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Erica Yegella, amesema hafla hiyo imekuwa sehemu ya utamaduni wa Halmashauri hiyo kuwakutanisha wadau mbalimbali wakiwemo viongozi wa dini na wafanyabiashara ili kuimarisha ushirikiano katika kuleta maendeleo ya wilaya.

Hii ni mara ya pili kwa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya kuandaa Iftari kwa ajili ya watumishi na wananchi, hatua inayotajwa kusaidia kupunguza mwanya kati ya watendaji wa serikali na jamii wanayoihudumia.








Jumla ya miti 1,500 ya matunda na kivuli imepandwa leo katika Shule ya Msingi Msinjahili, Manispaa ya Lindi, ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha utunzaji wa mazingira na kujiandaa na maadhimisho ya Siku ya Misitu Duniani pamoja na Wiki ya Upandaji Miti Kitaifa itakayofanyika mkoani Lindi.

Zoezi hilo limeongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Lindi, Victoria Mwanziva, ambaye amewahimiza wananchi, wanafunzi na taasisi mbalimbali kuendelea kushiriki kikamilifu katika kampeni ya upandaji miti ili kulinda mazingira na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Mwanziva amesema kuwa miti ina mchango mkubwa katika kuhifadhi mazingira, kuboresha hali ya hewa na kutoa manufaa mbalimbali ikiwemo matunda, kivuli na malighafi muhimu kwa jamii. Amesisitiza kuwa kila mwananchi ana wajibu wa kupanda na kuitunza miti ili kuhakikisha mazingira yanabaki salama kwa kizazi cha sasa na kijacho.

Akieleza kuhusu kampeni ya upandaji miti pamoja na maandalizi ya maadhimisho ya upandaji miti kitaifa, Saimoni Kipeleja kutoka Idara ya Misitu na Nyuki ya Wizara ya Maliasili na Utalii amesema serikali inaendelea kuhamasisha upandaji miti nchini kama sehemu ya mkakati wa kuongeza uoto wa asili na kukabiliana na uharibifu wa mazingira.

Kipeleja amesema kuwa maadhimisho hayo yanatarajiwa kuwakutanisha wadau mbalimbali wakiwemo viongozi wa serikali, taasisi, wanafunzi na wananchi kwa lengo la kuhamasisha upandaji miti na kuimarisha juhudi za uhifadhi wa misitu.

Awali, Mhifadhi wa Wilaya ya Lindi kutoka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Gaspar Vicent, amesema taasisi hiyo imekuwa ikizalisha miche ya miti zaidi ya laki mbili kila mwaka na kuigawa kwa taasisi mbalimbali pamoja na watu binafsi ili kuongeza kasi ya upandaji miti katika jamii.

Vicent amebainisha kuwa ushirikiano wa wananchi ni muhimu katika kuhakikisha miti inayopandwa inatunzwa ipasavyo ili kufikia malengo ya kuongeza uoto wa asili na kulinda rasilimali za misitu. Zoezi hilo la upandaji miti limehudhuriwa na viongozi wa serikali, walimu, wanafunzi pamoja na wadau wa mazingira. 

Maadhimisho ya Siku ya Misitu Duniani na Kampeni ya upandaji miti Kitaifa yanaenda sambamba na Kauli mbiu isemayo Misitu ni uchumi endelevu,Tuhifadhi kwa Maendeleo ya Taifa.










Top News