📍Yasifu uwekezaji wa shilingi bilioni 429


NA MASHAKA MHANDO, Tanga

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu imeiashauri Serikali kuongeza kasi ya utatuzi wa changamoto za miundombinu wezeshi katika Bandari ya Tanga, ili kuendana na kasi ya ongezeko la shehena na meli kubwa zinazoingia bandarini hapo kufuatia maboresho makubwa yaliyofanyika.

Ushauri huo umetolewa Leo Machi 13 na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Profesa Joyce Ndalichako, wakati wa ziara ya kikazi ya kukagua utendaji na ufanisi wa bandari hiyo, ambayo hivi sasa imekuwa mbadala muhimu katika kupunguza msongamano wa mizigo kwenye Bandari ya Dar es Salaam.

Akizungumza baada ya kukagua gati jipya, Profesa Ndalichako alipongeza uwekezaji wa Shilingi Bilioni 429 uliowekwa na Serikali ya Awamu ya Sita, akisisitiza kuwa ni lazima kasi ya ujenzi wa barabara za kuingia na kutoka bandarini iongezwe ili kurahisisha usafirishaji wa mizigo kwenda kwa walaji.

“Kamati inampongeza Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa maono yake ya kuifungua Tanga. Tunaunga mkono mpango wa kuunganisha bandari hii na reli ya kisasa ya SGR kutoka Tanga hadi Musoma, hatua itakayochochea tija na ajira kwa wingi,” alisema Profesa Ndalichako.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Uchukuzi,  David Kihenzile, alibainisha kuwa Serikali inaendelea na mpango wa kuunganisha bandari hiyo na mtandao wa reli wa kilomita 248 (Tanga–Mruazi–Ruvu) na hatimaye kufika Arusha. Alieleza kuwa reli ya SGR kupitia Minjingu na Engaruka hadi Musoma itakuwa kiunganishi muhimu cha kiuchumi.

Meneja wa Bandari ya Tanga,  Salehe Mbega, alieleza kuwa maboresho hayo yameongeza kina cha maji kufikia mita 12, hali inayoruhusu meli kubwa zenye urefu wa hadi mita 200 kutia nanga, tofauti na hapo awali.

“Ufanisi umeongezeka kiasi kwamba meli sasa zinahudumiwa ndani ya siku tatu hadi tano. Hata hivyo, kutokana na ubora wa huduma zetu, mahitaji yameongezeka na wakati mwingine hadi meli 14 husubiri nje ya bandari. Ili kutatua hili, tuna mpango wa kujenga magati matatu mapya na kituo cha kisasa cha abiria (Terminal) katika awamu ya tatu ya mradi,” alisema Mbega.

Maboresho hayo yanatajwa kuwa kichocheo kikubwa cha uchumi wa mkoa wa Tanga, yakigusa sekta za usafirishaji, biashara ndogondogo, na kuimarisha nafasi ya mkoa huo kama kitovu cha uwekezaji nchini. 







Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rose Senyamule, ametoa wito kwa wazazi na walezi kuwa makini na watoto wao wakati wa msimu wa mvua ili kuepuka ajali zinazoweza kusababisha vifo, kufuatia watoto wawili wadogo kufariki dunia baada ya kuzama kwenye madimbwi ya maji.

Akizungumza wakati wa ziara yake ya kukagua maeneo yaliyoathiriwa na mvua Kata ya Nzuguni Halimashauri ya Jiji la Dodoma, leo Machi 13, 2026, amesema ni muhimu kwa wazazi kuhakikisha watoto hawachezi kwenye madimbwi au maeneo yenye maji mengi kipindi hiki cha mvua ili kuwalinda dhidi ya hatari zinazoweza kutokea.

Aidha, amewataka wananchi kutunza mazingira na kuepuka kuchafua mifereji ya maji kwa kutupa taka ovyo, akieleza kuwa hali hiyo huchangia kuziba mifereji na kusababisha maji kujaa katika makazi ya watu pamoja na barabarani.

Amesema pamoja na changamoto zinazosababishwa na mvua, bado wananchi wanapaswa kuona kuwa mvua ni neema kwa Jiji la Dodoma kwa kuwa inaongeza uzalishaji wa chakula na kuleta ukijani kwenye mazingira.

Katika hatua nyingine, amewataka baadhi ya wananchi waliovamia na kujenga kwenye njia za maji kuzingatia sheria za mipango miji ili kuepusha madhara yanayotokea wakati wa mvua, ikiwemo nyumba kujaa maji.

Ametoa pole kwa wananchi waliokumbwa na athari za mvua na kuwataka kuwa na uvumilivu wakati Serikali ikiendelea na jitihada za kutatua changamoto hizo. Amesema suluhisho la kudumu litatekelezwa mara mvua zitakapopungua kunyesha ili kuruhusu utekelezaji wa maboresho ya miundombinu ya barabara na mifereji ya maji.

Akisoma taarifa kwa Mkuu wa Mkoa, Mtendaji wa Kata ya Nzuguni, Edgar Fungo, amesema kuanzia Januari 21, 2026 hadi Machi 13, 2026, jumla ya kaya 271 zimeathirika na maafa ya mvua katika kata hiyo. Kati ya hizo, nyumba 42 zimeezuliwa na upepo, nyumba 170 zimeingiliwa na maji na nyumba 59 zimebomoka.

Ameeleza kuwa mvua kubwa iliyonyesha Februari 9, 2026 iliathiri maeneo ya Mtaa wa Kitelela, Nzuguni C na Mahomanyika ambapo katika eneo la Kitelela barabara ziliharibika na kusababisha kushindwa kupitika, hali iliyosababisha wanafunzi kushindwa kwenda shule baada ya korongo kujaa maji pamoja na wananchi kukosa huduma za msingi.

Kwa upande wa Mahomanyika, daraja lilivunjika na kusababisha shughuli mbalimbali kusimama, huku katika eneo la Nzuguni C mfereji wa maji uliochimbwa kuzunguka ukuta wa Nane Nane ulijaa na kusababisha maji kusambaa hadi kwenye makazi ya wananchi.

Aidha, amesema Mbunge wa Jimbo la Mtumba, Anthony Mavunde, kwa kushirikiana na uongozi wa kata pamoja na diwani wa kata hiyo walitembelea maeneo yaliyoathirika na kutoa pole kwa wananchi pamoja na kusikiliza changamoto zao.

Amesema ushirikiano kati ya Serikali, viongozi wa eneo pamoja na taasisi mbalimbali ni muhimu katika kuhakikisha wananchi wanaopata madhara wanapatiwa msaada na hatua za kudumu zinachukuliwa ili kupunguza athari za mafuriko katika maeneo hayo siku zijazo.




‎Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga amewataka watumishi wa Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) mkoani Singida kutambua kuwa sekta ya barabara ni kiungo muhimu cha maendeleo ya sekta nyingine kama elimu, afya na uchumi, hivyo wanapaswa kutekeleza majukumu yao kwa bidii na weledi ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora.

‎Ameyazungumza hayo leo 13 Machi 2026, katika kikao kazi cha TARURA kilichofanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Ukaguzi mkoa wa Singida ambapo Dkt. Mganga amesema TARURA ni taasisi mtambuka na inategemewa na sekta nyingi, hivyo utekelezaji mzuri wa majukumu yao ni muhimu kwa maendeleo ya jamii.

‎Amesema moja ya changamoto kubwa inayowakabili wananchi ni uwepo wa barabara zisizopitika, hivyo watumishi wa TARURA wanapaswa kuhakikisha wanakuwa karibu na maeneo ya kazi hasa katika kipindi cha mvua ili kufuatilia hali ya barabara na kuhakikisha zinaendelea kupitika.

‎‎Pia, amesisitiza umuhimu wa watumishi wa umma kuzingatia maadili ya utumishi wa umma, kuwa na mawasiliano mazuri na kuwahudumia wananchi kwa heshima akisisitiza kuwa “mteja ni mfalme”. 

Aidha, amewakumbusha watumishi kupambana na vitendo vya rushwa, kuheshimu muda wa kazi na kujaza taarifa katika mfumo wa PEPMIS ili kufikia malengo ya utendaji kazi.

‎Dkt. Mganga pia amesisitiza umuhimu wa watumishi wa umma kutunza afya zao kwa kufanya mazoezi, kupima afya mara kwa mara na kuepuka matumizi ya pombe kupita kiasi, akieleza kuwa serikali inawekeza rasilimali nyingi katika kuwajenga watumishi wake hivyo wanapaswa kulinda afya zao ili kuendelea kulitumikia taifa.

‎Awali, Meneja wa TARURA Mkoa wa Singida, Mhandisi Claver Mwinuka, amesema kikao kazi hicho kinalenga kujadili mipango ya kazi, bajeti ya mwaka ujao wa fedha pamoja na mikakati mipya ya utekelezaji wa majukumu kwa kuzingatia maelekezo ya Bodi ya Barabara mkoa wa Singida.

‎Ameongeza kuwa kikao hicho pia kitatoa fursa ya kuimarisha mahusiano na mawasiliano kati ya watumishi, hususani wapya pamoja na kujadili matumizi ya teknolojia ya mawe katika ujenzi wa barabara ili kupunguza gharama na kuboresha ubora wa miundombinu.

‎Baadhi ya washiriki wa kikao hicho wakiwemo Meneja wa TARURA Wilaya ya Iramba Mhandisi Evance Kibona na Meneja wa TARURA Wilaya ya Mkalama Mhandisi Rahabu Thomas, wamesema kikao hicho kitasaidia kuboresha utendaji kazi na kuongeza ubunifu katika ujenzi wa barabara, hususani kwa kutumia rasilimali za mawe zinazopatikana kwa wingi mkoani Singida ili kuongeza ubora wa barabara na kurahisisha usafirishaji wa mazao ya kilimo.











MKUU wa Wilaya ya Ubungo, Albert Msando amesema amekabidhi magari mawili kwa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) ikiwa ni muendelezo wa jitihada zinazokufanywa na serikali katika kuhakikisha inaimarisha miundombinu na kuongeza ufanisi na uhakika wa upatikanaji wa huduma ya nishati ya umeme nchini.

Msando amekabidhi magari hayo leo wilayani Ubungo mkoani Dar es Salaam, kwa Meneja wa TANESCO Wilaya ya Kinondoni Kusini, ambako amesema usafiri huo utaenda kuongeza chachu ya utoaji hudu ikiwemo kuwawezesha watumishi kufika kwa wakati katika maeneo yenye changamoto.

Amesema hatua hiyo ni moja ya utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na maono ya Rais Samia Suluhu Hassan, katika kuendelea kuboresha huduma ya umeme, na kwamba ili shirika liendelee kutoa huduma bora ni lazima liwe na vitendea kazi vitakavyowasaidia katika utekelezaji wa majukumu yao.

"Tunaishukuru serikali chini ya Rais samia kwa kuliwezesha shirika kupata vifaa hivi muhimu katika utendaji wao, sisi kama Wilaya ya Ubungo tutahakikisha vifaa hivi vinasimamiwa vizuri ili viweze kuleta tija katika eneo letu, ikiwemo kufika kwa haraka kwenye maeneo ya utoaji huduma kwa wananchi," amesema Msando.

Ameongeza kuwa vifaa vyenye ubora na ufanishi ni muhimu sana katika utendaji na usimamizi wa shughuli za TANESCO, na kwamba wanaamini kuwa watendaji wataenda kusimamia vizuri vifaa hivyo na kuwawezesha kuongeza tija kwenye utoaji huduma kwa jamii.

Aidha, ameeleza kuwa hayo yote yanafanyika kwasababu serikali iliahidi kuendelea kuboresha huduma ya umeme, mijini na vijijini, akisema Rais anathibitisha hilo kwa vitendo kufikia malengo ambayo wamejiwekea kama taifa.

"Nimpongeze Mkurugenzi Mkuu wa TANESCO, Lazaro Twange na timu yake kwa namna ambavyo wanaendelea kufanya kazi nzuri ya utoaji huduma kwa wananchi, malalamiko mengi kuhusu shirika hilo katika wilaya hetu yameondoka, pale inapotokea changamoto wamekuwa wepesi sana kufika kwa wakati eneo la tukio," amesema Msando.

Meneja wa TANESCO Mkoa wa Kinondoni Kusini, Adam Abdullah, ameishukuru serikali kwa kuwapatia magari hayo, akisema yatawasaidia katika utekelezaji wa miradi yao na kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora ya umeme kwa wananchi.

"Tutoe ahadi kwamba magari haya tutayatunza na kuhakikisha tunafikia malengo yetu hasa katika mkoa wetu wa Kinondoni Kusini," amesema Abdullah.




Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Hamza Johari leo Machi 13, 2026 ameapishwa kuwa Kamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, katika hafla fupi ya uapisho iliyofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Jijini Dodoma.

Johari ameapa mbele ya Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, George Masaju, kufuatia kuteuliwa kuwa Mjumbe wa Tume hiyo.

Mwanasheria Mkuu wa Serikali ameteuliwa pia kuwa mjumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama kufuatia kuteuliwa kwake kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa mara ya pili na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan Novemba, 2026.

Aidha, Johari ameapishwa kuwa Kamishna kutimiza takwa la Sheria ya Usimamizi wa Mahakama Na. 4 Sura ya 237 inayomtaka kila Kamishna kuapishwa na Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama kabla ya kuanza kutekeleza majukumu yake.

Sambamba na Johari, Wajumbe wengine wa Tume ya Utumishi wa Mahakama walioapishwa ni pamoja na Jaji wa Mahakama ya Rufaa Gerson Mdemu, na Mawakili wa Kujitegemea Thomas Nyanduga na Dorcas Mutabuzi.

Wizara ya Nishati kupitia Katibu Mkuu anayeshughulikia masuala ya mafuta na gesi asilia Dkt. James Mataragio imekutana na Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) kwa lengo la kujadili na kuweka mikakati ya kuimarisha shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi asilia nchini.

Kikao hicho kilichofanyika Machi 12, 2026 Jijini Dar es Salaam kilihudhuriwa na Kamishna Msaidizi wa Petroli kutoka Wizara ya Nishati Mhandisi Antelimi Raphael, Mkurugenzi Mkuu wa PURA Mhandisi Charles Sangweni na baadhi ya viongozi kutoka Wizara ya Nishati na PURA.

Akizungumza katika ufunguzi wa kikao hicho, Dkt. Mataragio alieleza kuwa miongoni mwa masuala yanayohitaji kufanyiwa kazi kubwa katika sekta ya mafuta na gesi ni eneo la utafutaji wa mafuta na gesi asilia nchini kwa kuzingatia kuwa shughuli hizo zimepungua kwa kiasi kikubwa.

“Miaka ya nyuma, shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi asilia nchini zilikuwa zikifanyika kwa wingi na kasi kubwa. Tukiangalia hata mikataba ya uzalishaji na ugawanaji wa mapato yani PSA, zilikuwa zaidi ya 26 lakini leo hii tunaongelea mikataba 11 pekee”

“Na ukijaribu kuangalia kwa kina, hata katika PSA zilizobaki, ni kampuni chache zinatekeleza majukumu yao ya kuendelea kufanya utafutaji wa mafuta na gesi asilia. Hali hili hairidhishi. Lazima tuweke mikakati inayolenga kuchochea shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi asilia nchini” alisema Dkt. Mataragio.

Alibainisha kuwa mdororo wa shughuli za utafutaji ni hatari kwa uhakika wa upatikanaji wa gesi asilia kwa kuwa utafutaji ndio chachu ya ugunduzi ambao ukiendelezwa unapelekea uzalishaji wa gesi asilia.

“Kwa sasa tumejipanga kama Wizara kuhakikisha tunaweka jitihada kubwa katika eneo hili na kuweka mazingira wezeshi kwa ustawi wa shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi asilia” aliongeza Dkt. Mataragio.

Kwa upande wake, Mha. Charles Sangweni alieleza kuwa PURA imeendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuendeleza shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi asilia nchini.

Miongoni mwa mikakati hiyo ni pamoja na kuingia mikataba na makampuni ya kijiofizikia yaliyobobea katika ukusanyaji wa data za petroli (Multi Client Geophysical Companies) kwa lengo la kuendeleza utafiti katika maeneo ya bahari kuu na nchi kavu.

Kupitia kikao hicho, Wizara ya Nishati na PURA zilijadili kwa kina mikakati ya kuimarisha shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi asilia na kuainisha masuala muhimu yanayopaswa kufanyiwa kazi haraka ili kuleta uhai katika sekta.






Na Oscar Assenga,TANGA

Kamati ya kudumu ya Bunge ya miundombinu leo imefanya ziara ya kutembelea Bandari ya Tanga huku ikiridhinshwa na uboreshaji wa miundombinu katika Bandari ya Tanga hatua inayoonesha mabadiliko ya kiutendaji ikiwemo ongezeko la shehena za mizigo.

Hayo yalisemwa leo na Mwenyekiti wa Kamati hiyo Profesa Joyce Ndalichako wakati wa ziara hiyo katika Bandari ya Tanga ambapo alisema maono ya Serikali yameleta mapinduzi katika Bandari ya Tanga na wao kama wasimamizi wataendelea kuisimamia Serikali katika utekelezaji wa mradi huo

Uboresho huo wa Bandari ya Tanga umepelekea kuvuka lengo la upokeaji wa shehena za mizigo kutoka mataifa mbalimbali kutoka tani 137,000 mwezi Oktoba hadi kufikia tani zaidi ya 200,000 mwezi Novemba mwaka 2025.

Alisema kutokana na maboresho hayo wana kila sababu ya kuipongeza Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Raisi Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uboreshaji wa Bandari ya Tanga hatua inayochagiza kuinua uchumi wa mkoa wa Tanga kwa kiasi kikubwa.

Profesa Ndalichako alisema kwamba uwekezaji huo wa shilingi bilioni 429.1 uliofanywa na Serikali katika Bandari ya Tanga umewezesha uchimbwaji wa kina na ujenzi wa gati hatua iliyoiongezea ufanisi wa utendaji na hivyo kuwezesha meli kubwa kutia nanga na kurahisisha shughuli za upakiaji na upakuaji wa mizigo.

Aliongeza Serikali ina maono ya kuunganisha Bandari na reli ambapo mpango uliopo ni kujenga reli ya kisasa ya SGR kutoka Tanga hadi Musoma hatua itakayochochea maendeleo ya mkoa wa Tanga na kuzalisha ajira kwa vijana.

Kamati ya kudumu ya Bunge ya miundombinu imeipongeza Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Raisi Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uboreshaji wa Bandari ya Tanga hatua inayochagiza kuinua uchumi wa mkoa wa Tanga kwa kiasi kikubwa.

Uwekezaji wa shilingi bilioni 429.1 uliofanywa na Serikali katika Bandari ya Tanga zimewezesha uchimbwaji wa kina na ujenzi wa gati na hatimaye kuleta ufanisi wa utendaji katika Bandari hiyo hatua inayowezesha Meli kubwa kutia nanga na kurahisusha shughuli za upakiaji na upakuaji wa mizigo.

Aidha katika hatua nyengine Profesa Ndalichako amesema Serikali ina maono ya kuunganisha Bandari na reli ambapo mpango uliopo ni kujenga reli ya kisasa ya SGR kutoka Tanga hadi Musoma hatua itakayochagiza maendeleo ya mkoa wa Tanga hususani kwa vijana kupata ajira.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile, alisema Serikali inaendelea na mpango wa kuunganisha bandari hiyo na mtandao wa reli wa kilomita 248 (Tanga–Mruazi–Ruvu) na hatimaye kufika Arusha.

Alisema pamoja na kuwa na reli ya SGR kupitia Minjingu na Engaruka hadi Musoma itakuwa kiunganishi muhimu cha kiuchumi.

Naye kwa upande wake ,Meneja wa Bandari ya Tanga, Salehe Mbega alisema maboresho hayo yameongeza kina cha maji kufikia mita 12 hali inayoruhusu meli kubwa zenye urefu wa hadi mita 200 kutia nanga gatini tofauti na hapo awali.

Na Said Mwishehe,Michuzi TV

LEO naomba unipe nafasi kidogo tuzungumze kuhusu Wakala wa Nishati Vijijini (REA) ambayo ni taasisi ya serikali ya Tanzania iliyoanzishwa chini ya Wizara ya Nishati.

Jukumu namba moja la REA ni kusimamia na kurahisisha upatikanaji wa nishati bora na ya uhakika (hasa umeme) katika maeneo ya vijijini ili kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Nimeanza na kuilezea REA kwa kifupi ili unaposoma nilichoandika basi uelewe nazungumza kuhusu nini. Ndio maana najua wapo ambao hawajui REA ni nini na inafanya kazi gani nchini kwetu Tanzania.

Ngoja nikueleze kwa lugha rahisi zaidi iko hivi ukiona kijijini umeme unawaka katika nyumba ya bibi au babu,baba mkubwa au baba mdogo ,Shangazi au Mjomba kule kijijini basi ujue waliofikisha na kusamabaza umeme huo ni REA.


REA kila wanapolala na kuamka wao wanafikiria ni kwa namna gani umeme utafika katika vijiji vyetu,iwe kijiji cha kule Mpitimbi,iwe kijiii cha Madunda kule Ludewa au kule kwa Mpiga Miti wilayani Liwale.

Yaani ukiona umeme kijijini kwenu ujue hao ndio REA sasa .Hata ukiwa kule Oldonyosambo na umeme ukawa unawaka hao ni REA .Nadhani tumeelewa.Usiichukulie poa kabisa.Nakwambia ukweli.Wee cheka tu kama hamnazo.

Ikumbuwe nchini Tanzania tunavyo vijiji 12,364 na Vitongoji 64539na kote huko REA wapo kazini kwa ajili ya kufikisha nishati bora ya umeme na kwa kazi nzuri ambayo wameendelea kuifanya vijiji vyote vina umeme na kazi sasa inaendelea katika vitongoji.

Hata hivyo naomba iweleke katika hivyo vitongoji ambavyo nimevitaja hapo juu tayari vingine vina umeme, lengo ni kuwezesha wananchi waliko huko wanapata nishati ya umeme kama walioko mijini. Ukweli REA wameendelea kubadilisha maisha ya wananchi wa vijijini. Huo ndio ukweli maana kijiji chochote unachotaka kwenda umeme upo.

Zile mechi zetu za Simba na Yanga,Mtibwa na Kagera Sugar au Singida BS na Azam unaziona hata ukiwa kule Kijiji Kilumbi au Mwamalugu kule wilayani Sikongone mkoani Tabora utaziona mechi vizuri ukiwa katika Kibanda umiza kwa kuwa REA wapo kazini .

Unaposikia vijiji vyote vina umeme basi kichwani kwako ujue kuna mabilioni ya fedha yametumika. Serikali inatumia fedha nyingi kuhakikisha wananchi wanapata umeme. Nitoe mfano halisi kujenga kilometa moja ya umeme wa Msongo wa kati(33kv) inagharimu zaidi ya Sh.milioni 25.

Ukiona laini ya umeme yenye urefu wa kilometa 100 ujue gharama iliyotumika hapo si chini ya Sh.bilioni 2.5. Na kiasi hicho cha fedha ni katika maeneo ambayo yanafika kwa urahisi katika kufikisha miundombinu ya umeme wa REA.Maeneo mengine gharama ni zaidi ya hiyo.

Kwa mfano hivi karibu nimepata nafasi ya kutembelea miradi ya REA katika Wilaya ya Ludewa mkoani Njombe.Ziara hiyo ilihusisha Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF)ambalo Mwenyekiti wake ni Deodatus Balile.

Tukiwa katika ziara hiyo tumeona ugumu ambao REA wanaupata kufikisha nguzo katika vijiji na vitongoji vya Wilaya hiyo.Pale Madunda kuna milima mirefu sana na mabonde lakini REA bila kujali ugumu wa Mazingira hayo wamefikisha nguzo katika vitongoji sıta vya Kitewele,Kimata , Kigulu,Chanjale Lumbira na Nkanda.

Msimamizi wa miradi ya REA Kanda ya Nyanda za Juu Kusini Mhandisi Danstan Kalugira anaeleza namna ambavyo REA imelazimika kuwatumia SUMA JK kusimika nguzo kwa umbali kilometa 36.69 za msongo wa kati na za msongo wa chini ni kilometa 15.06.

Katika mradi huo zitatumika mashine umba sita. Nimesema mashine unauliza mashine ndio nini?Acha mambo yako mashine umba kwa lugha tuliyozoea huku mtaani tunaita Transifoma.

Na idadi ya wateja watakaonufaika wa mwanzo ni 160, hivyo mradi ukikamilika wananchi changamkieni umeme wa REA.Nikwambie ukweli acha kulaza damu, kwani wee hutaki kuangalia vipindi vya Azam TV hasa Chanel ya Sinema? Kwani hupendi kuangalia taarifa ya habari ya Alasiri,Aridhio au habari ya saa mbili usiku?Changamka wewe 🤣🤣

Wakati wa ziara hiyo pia tumeona namna ambavyo REA imewakaribisha wawekezaji na mashirika binafsi kuwekeza katika kuzalisha umeme vijijini kupitia vyanzo vya maji. Kwa Wilaya ya Makete tumeona mradi wa kuzalisha umeme wa Ijangala uliopo wilayani Makete mkoani Njombe.

Mradi huo unazalisha megawati 360 na utaunganishwa katika gridi ya Taifa.Mradi huo unasimamiwa na Kanisa la Kiinjili la Kulutheri Tanzania(KKKT)Kusini Kati. REA imetoa fedha ya ruzuku Sh.bilioni 1.63 kuufanikisha mradi huo.

Lakini kupitia mpango wa upanuzi wa umeme vijijini Tanzania (TREEP) mradi huo umepata Mkopo nafuu wa Sh. Milioni 922 kusaidia shughuli mbalimbali za utekelezaji wake.

Kwa Wilaya ya Njombe Kudewa Jukwaa la Wahariri pia limeona mradi wa kuzalisha umeme wa Lupali wenye uwezo wa kuzalisha megawati 317 ambapo REA imetoa fedha ya ruzuku Sh.bilioni 5.3 .Ni mradi unatekelezwa na Shirika la Benedictine Sisters of St.Gertrude Convint Imilawaha .

Ukifika katika mradi huo utaona REA ilivyokuwa siriazi katika kusambaza nishati ya umeme vijijini na kwenye vitongoji .Lakufurahisha zaidi wenye dhamira ya kweli wakala huo upo tayari kushirikiana nao kwa kila hatua.REA bwana wala hawana baya mtu.

Kaimu Meneja Usaidizi wa kifundi kwa waendelezaji kutoka REA Mhandisi Emmmanuel Yassaya anatumia nafasi hiyo kulieza Jukwaa la Wahariri kwamba imefungua milango kwa sekta binafsi kuwekeza katika kuzalisha nishati hiyo.

Hata hivyo kutokana na kazi kubwa na nzuri ambayo imefanywa na REA, Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania Deodatus Balile anatoa pongezi kwa REA kwa jinsi ilivyodhamiria kupeleka umeme vijijini.

Balile anasema hapo miaka ya nyuma kidogo ukiwa unasafiri moja ya alama ya kujua umefika mjini ni uwepo wa taa lakini sasa ni tofauti kwani vijiii vyote vina umeme .Ukienda kwa staili ya zamani utapotea.Usicheke mtu wangu.

Na hapo sijazungumzia ule mradi wa kusambaza gesi asilia majumbani ili wananchi wapike kwa nishati safi.Ni mradi ambao umetekelezwa katika mikoa ya Lindi na Pwani na tayari watu 1000 wanatumia nishati safi ya kupikia.

Nenda Kisevule Centre pale wilayani Mkurunga kisha muulizie dada Mariam Rashid atakwambia anavyoinjoi kupika kwa gesi aliyofungiwa bure na Serikali kupitia REA.Ni mradi uliogharimu Sh.bilioni sita.

Pamoja na hayo yooooote niliyoeleza jambo la msingi la kuzingatia kwa wananchi ni vema wakaheshimu na kutunza miundombinu ya REA kwani fedha nyingi zimetumika.

Kumekuwa na tabia kuharibu miundombinu aidha kwa kuiba waya au kuchoma nguzo .Wapo wengine wanaiba transfoma ili kwenda kuuza kama Skrepa.Tuache tabia hiyo.

Kuwa mzalendo kwa kulinda miundombinu ya REA na kila mmoja wetu akawa mlinzi kwa mwenzake.Hata hivyo wakati wa Mjini unasema REA wa nini walioko katika vitongoji wanasema REA itakuja lini.?

Nikutakie mfungo mwema wa Ramadhani, mfungo mwema wa Kwaresma.Halafu nimeshanunua Abaya la wifi yenu kwa ajili ya Sikukuu ya Eid wakati naivutia kasi Pasaka. Alamsiki swahiba.



Ni mimi 0713833822/0762451570.
Equity Bank Tanzania imewateua Bi. Malik na Bi. Tarimo kwenye Bodi ya wakurugenzi na inatarajia kufaidika na ujuzi wao mkubwa huku Benki ikiendelea kuimarisha jukumu lake katika kukuza ushirikishwaji wa kifedha, kusaidia biashara ndogo na za kati, na kuleta ukuaji endelevu wa kiuchumi Tanzania.

Akizungumzia uteuzi huo, Dkt. Florens Martin Turuka, Mwenyekiti wa Equity Bank Tanzania, alisema: "Tunafuraha kuwakaribisha Fauzia Malik na Angelica Tarimo kwenye Bodi ya Equity Bank Tanzania. Uzoefu wao mkubwa katika ujasiriamali, utawala bora, na uongozi wa kimkakati utaongeza thamani kubwa kwenye Bodi tunapoendelea kuongoza ukuaji na mageuzi ya Benki yetu."

Kwa uteuzi huu, Bodi sasa ina jumla ya wanawake watano kati ya wakurugenzi, ikiangazia uongozi wa Equity Bank Tanzania katika kuendeleza usawa wa kijinsia na utawala jumuishi katika sekta ya huduma za kifedha nchini Tanzania.



Top News