Moshi, Tanzania

GGML Kili Challenge inayotekelezwa kupitia GGML Kili Trust, inashiriki Kilimanjaro Marathon 2026, maarufu kama “Mbio za Watu”, kupitia maonesho yanayofanyika katika viwanja vya Ushirika, Moshi, yaliyoanza tarehe 20 na kuendelea hadi 22 Machi. 

GGML Kilimanjaro Challenge Against HIV/AIDS ni mpango wa kuhamasisha ushiriki wa wadau mbalimbali katika mapambano dhidi ya UKIMWI nchini. Kupitia GGML Kili Trust, rasilimali hukusanywa na kuelekezwa kwenye miradi inayonufaisha moja kwa moja watu wanaoishi na VVU pamoja na taasisi zinazowahudumia. Mwaka huu, Kili Trust imeanza kushirikiana kwa karibu zaidi na asasi za kiraia kutoka maeneo mbalimbali nchini zinazotekeleza programu za kusaidia watu walioathiriwa na VVU na UKIMWI, hatua inayolenga kuongeza ufanisi na kufikia watu wengi zaidi.

Kupitia banda la GGML Kili Challenge, washiriki wa mbio na wageni wa maonesho wanapata fursa ya kujifunza zaidi kuhusu GGML Kili Challenge, namna ya kushiriki, pamoja na miradi inayotekelezwa chini ya mfuko huo.

Huduma za upimaji wa VVU pia zinatolewa  moja kwa moja katika banda hilo kwa kushirikiana na wadau wa kitaifa, Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania, kwa lengo la kuendelea kuhamasisha uelewa na hatua za kinga. Aidha, wageni wanaweza kutoa ahadi ya kuchangia, kujisajili kushiriki GGML Kili Challenge, mnamo Julai 2026, na kupata maelezo kuhusu njia mbalimbali za kushiriki katika mapambano haya.

Tangu kuanzishwa mwaka 2002, mpango huu umeendelea kuleta watu binafsi, taasisi na washirika pamoja kuchangia jitihada za kinga, tiba, matunzo na msaada kwa jamii.

Akizungumza kuhusu ushiriki huo, Meneja wa GGML Kili Trust, Stephen Mhando, amesema juhudi za mfuko huo zinalenga kuunga mkono mikakati ya taifa katika kupambana na UKIMWI kupitia ushirikiano na uhamasishaji wa jamii.

“Tunawaalika washiriki wote wa marathon na wageni wa maonesho kutembelea banda la GGML Kili Challenge ili kujifunza zaidi na kuona namna wanavyoweza kushiriki, iwe kama mtu binafsi au taasisi, katika kuunga mkono jitihada hizi.”

Kupitia ushiriki huu, GGML Kili Trust inaendelea kusisitiza umuhimu wa kufikia malengo ya sifuri tatu, yaani maambukizi mapya sifuri, unyanyapaa sifuri, na vifo vitokanavyo na UKIMWI sifuri.






-Watanzania waaswa kulinda amani

Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa leo Machi 21, 2026 ameungana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na waumini wa dini ya Kiislam kwenye Swala ya Eid El-Fitri katika Msikiti Mkuu wa BAKWATA (Mfalme Mohamed VI), Kinondoni, jijini Dar es Salaam.


Ibada hiyo ya kitaifa iliyoongozwa na Sheikh Mkuu wa Tanzania Mufti Abubakar Bin Zubeir, inayofanyika mara baada ya kumalizika kwa siku 30 za mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhan Machi 20, 2026



Pia ibada ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni Mhe. Saad Mtambule.



Katika ibada hiyo Sheikh Mkuu wa Tanzania Mufti Abubakar Bin Zubeir, amehimiza amani, umoja na mshikamano kwa waumini wa kiislam na watanzania kwa ujumla.



Na. Mwandishi Wetu.

Awamu ya Tatu ya Mradi wa Mabasi Yaendayo Haraka maarufu kama Mwendokasi katika Barabara ya Nyerere kuelekea Gongolamboto na maeneo yaJirani sasa umefikia asilimia 99 kwa ujenzi wa Vituo vya Mabasi Pamoja na Barabara za zege.

Akizungumza kuhusu maendeleo ya awamu hiyo Kaimu Mkurugenzi wa Maendeleo ya Usafirishaji wa Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka Bi. Delphina Pweleza amesema kuwa ujenzi wa awamu hiyo ya tatu ya BRT uligawanyika katika Lot 2 yaani ujenzi wa miundombinu ya Barabara na Vituo vyake ambao mpaka sasa umefikia asilimia 99% huku Lot ya 2 inayohusisha ujenzi wa Karakana, Kituo Kikuu cha Airport na kituo mlishi cha Banana ikiwa kwenye hatua za awali.

“Kwa sasa ujenzi wa miundombinu ya barabara na vituo umekamilika kwa asilimia tisini na tisa (99%) na matarajio ya kukabidhiwa ikiwa ni mwishoni mwa mwezi April 2026” Alisema Bi. Pweleza.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wakazi wa Gongolamboto Jijini Dar es Salaam wamesema mradi huo utakapoanza kufnya kazi utakuwa mkombozi mkubwa katika usafiri wa umma kwani wameusubiri kwa muda mrefu.

“Tunaishukuru Serikali ya Dkt Samia kwa kuendelea kujenge miundombinu ya kimkakati kama hii ambayo lengo lake kubwa ni kutuondolea kero ya usafiri sisi wakazi wa Gongolamboto, Pugu, KIsarawe na maeneo ya Jirani” Alisema Hamad Shelukindo Mkazi wa Pugu Kajiungeni JIjini Dar es Salaam.

Naye Anselim Obeid wa Ukonga amesema mradi huo utakapoanza utawasaidia sana wakina mama na wanaunzi ambao mara nyingi wamekuwa wakihangaika na usafiri wa umma usio wa uhakika.

Awamu ya tatu ya mradi wa BRT kuelekea Gongolamboto inahusisha tawi lingine la Barabara linaloanzia kwenye Kituo Kikuu cha Mabasi Kariakoo Gerezani kupitia mitaa ya Lindi, Shaurimoyo na Uhuru hadi Buguruni inapoungana na Barabara ya Nelson Mandela na kujiunga na Barabara ya Nyerere kwenye makutano ya TAZARA ikiwa na urefu wa kilomita 23.6 ikiunganishwa na Awamu ya Kwanza na ya Pili ya mradi katika Vituo Vikuu vya Kariakoo - Gerezani na Kivukoni.

Aidha awamu ya tatu ujenzi unajumuisha barabara pekee za Mabasi (exclusive BRT lanes), barabara za magari binafsi, njia za waenda kwa miguu pamoja na baiskeli zenye jumla ya urefu wa kilomita 23.6, Vituo Vikuu na vidogo vya mabasi, karakana pamoja na vituo mlishi.

Ujenzi wa miundombinu ya Awamu ya Tatu ya Mradi wa DART unatekelezwa kwa ufadhili wa Benki ya Dunia kupitia Mradi wa Uboreshaji wa Hali ya Usafiri katika Jiji la Dar es Salaam (DUTIP).


JESHI la Polisi Mkoa wa Mbeya linapenda kutoa ufafanuzi wa tukio la kifo cha mtoto Nehemia Cheyo, miaka 13, aliyekuwa Mwanafunzi wa Darasa la Sita katika Shule ya Msingi Kiwira Coal Mine Wilayani Kyela ambaye alipotea na baadae kukutwa amefariki dunia katika Maporomoko ya Mto Lema.

Ni kwamba mnamo Machi 3, 2026 saa 11 jioni katika Kijiji cha Lema kilichopo Kata ya Busale, Tarafa ya Unyakyusa, Wilaya ya Kyela, Mkoa wa Mbeya, mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la Jackson Cheyo, miaka 46, mkazi wa Kijiji cha Lema aligundua kuwa mtoto wake aitwaye Nehemia Cheyo, miaka 13 amekufa maji katika maporomoko ya Mto Lema baada ya kupotea tangu Februari 26, 2026

Kufuatia tukio hilo, Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya kupitia Askari wa kuchunguza matukio ya vifo, lilifika eneo la tukio na kuukuta mwili wa mtoto huyo na kuanza uchunguzi kwa kushirikiana na Daktari kutoka Hospitali ya Wilaya ya Kyela ambaye alibaini kuwa chanzo cha kifo ni kukosa hewa wakati alipokuwa katika jitihada za kujiokoa ndani ya maji na kupelekea kifo chake.

Katika uchunguzi uliofanywa na Daktari pamoja na Askari wa uchunguzi wa matukio, baba mzazi wa marehemu aitwaye Jackson Cheyo ni miongoni mwa walioshuhudia uchunguzi wa mwili wa mtoto baada ya kumtambua kuwa ni mtoto wake aitwaye Nehemia Cheyo ambaye pia alieleza kuwa Februari 26, 2026 saa 3 asubuhi watoto wake ambao ni Nehemia Cheyo ambaye kwa sasa ni marehemu na Fanikiwa Cheyo walirudi kutoka Shuleni wakidai hakuna masomo kutokana na Walimu kwenda kuhudhuria kikao.

Baba huyo aliendelea kueleza kuwa aliwatuma watoto wake kwenda kuokota maparachichi lakini baada ya nusu saa Fanikiwa Cheyo pekee ndiye aliyerudi na alipoulizwa alidai kuwa kaka yake amepita njia nyingine. Jitihada za kumtafuta zilifanyika lakini hakuonekana hadi Machi 3, 2026 mwili wake ulipokutwa katika eneo ambalo zamani lilikuwa Machimbo ya Makaa ya Mawe lakini kwa sasa kuna maporomoko ya maji ya Mto Lema akiwa amefariki dunia.

Chanzo cha kifo cha mtoto huyo kulingana na uchunguzi na Ushahidi uliokusanywa ni hicho tofauti na taarifa zilizotolewa na baadhi ya vyombo vya habari zikidai kuwa mtoto huyo aliuawa.

Jeshi la Polisi linamkaribisha yeyote mwenye Ushahidi tofauti na uliokusanywa hadi sasa asisite kuwasilisha.

Imetolewa na:
Kamanda wa Polisi,
Mkoa wa Mbeya.
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Pwani imekamata bidhaa mbalimbali za magendo katika Wilaya ya Bagamoyo ikiwemo viroba 50 vya mchele, madumu 10 ya mafuta ya kula na sabuni box 25 aina ya Malaika.

Kwa mujibu wa Meneja Msaidizi wa Forodha mkoa wa Pwani Bi. Melinda Matinyi bidhaa hizo za magendo zimekamatwa Machi 19.2026 kufuatia operesheni ya udhibiti wa bidhaa zinazoingizwa nchini au kusafirishwa bila kufuata taratibu za kisheria za forodha.

Amesema idhaa zilizokamatwa zimehifadhiwa katika yadi ya TRA Bagamoyo kwa ajili ya kuendelea na taratibu za kiforodha na hatua nyingine za kisheria.

Mamlaka ya Mapato Tanzania imeendelea kutoa wito kwa wafanyabiashara na wananchi kwa ujumla kufuata sheria na taratibu za kodi na forodha ili kuepuka hasara na adhabu zinazoweza kujitokeza pindi wanapojihusisha na vitendohivyo.


 

Mkuu wa Kanda ya Tume ya Ushindani (FCC) - Nyanda ya Juu Kusini, Bw. Dickson Mbanga,akitoa elimu kuhusiana madhara ya bidhaa bandia kwa wanafunzi wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Njombe (FDC) ikiwa ni sehemu ya kuelekea Maadhimisho ya Wiki ya Siku ya Haki za Mlaji Duniani 2026.

....

TUME ya Ushindani (FCC) kanda ya Nyanda za Juu Kusini  imetoa elimu kwa wanafunzi wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Njombe (FDC) kuhusu masuala ya kumlinda mlaji, ikiwemo haki na wajibu wa mlaji pamoja na madhara ya matumizi ya bidhaa bandia katika jamii.

Elimu hiyo imelenga kuwajengea wanafunzi uelewa mpana ili waweze kufanya maamuzi sahihi wanaponunua na kutumia bidhaa mbalimbali  ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Haki za Mlaji Duniani 2026.

Akitoa elimu hiyo Mkoani Njombe, Mkuu wa Kanda ya Tume ya Ushindani (FCC) Nyanda za Juu Kusini, Bw. Dickson Mbanga, amesisitiza umuhimu wa kila mlaji kufahamu haki zake za msingi.alieza kuwa haki hizo ni pamoja na kupata bidhaa bora, kupata taarifa sahihi kuhusu bidhaa, pamoja na haki ya kulalamika pale mlaji anapodhulumiwa.

Aidha, Bw. Mbanga ameeleza madhara makubwa yatokanayo na matumizi ya bidhaa bandia, akibainisha kuwa bidhaa hizo zinaweza kusababisha athari za kiafya, kupoteza fedha, na kudhoofisha uchumi wa nchi. Amewataka wanafunzi kuwa mabalozi wa kuelimisha jamii zao ili kupunguza matumizi ya bidhaa hizo hatarishi.

“FCC imesisitiza kuwa elimu hii ni endelevu na inalenga kuwafikia makundi mbalimbali ya jamii ili kujenga taifa lenye walaji wenye uelewa na uwezo wa kufanya maamuzi sahihi.”amesema Bw. Mbanga

Kwa ujumla, mafunzo hayo yameacha alama chanya kwa wanafunzi wa FDC Njombe, ambapo wengi wao wameeleza kuwa elimu hiyo imewafungua macho na kuwapa nguvu ya kusimamia haki zao kama walaji, huku wakiahidi kushiriki kikamilifu katika mapambano dhidi ya bidhaa bandia nchini.

Kupitia mafunzo hayo, walikumbushwa kuwa mlaji ana nafasi kubwa katika kulinda afya yake na uchumi wa taifa kwa kuchagua bidhaa zilizo salama na zenye ubora unaokubalika.

Mkuu wa Kanda ya Tume ya Ushindani (FCC) - Nyanda ya Juu Kusini, Bw. Dickson Mbanga,akitoa elimu kuhusiana madhara ya bidhaa bandia kwa wanafunzi wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Njombe (FDC) ikiwa ni sehemu ya kuelekea Maadhimisho ya Wiki ya Siku ya Haki za Mlaji Duniani 2026.

Mkuu wa Kanda ya Tume ya Ushindani (FCC) - Nyanda ya Juu Kusini, Bw. Dickson Mbanga,akitoa elimu kuhusiana madhara ya bidhaa bandia kwa wanafunzi wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Njombe (FDC) ikiwa ni sehemu ya kuelekea Maadhimisho ya Wiki ya Siku ya Haki za Mlaji Duniani 2026.

Mkuu wa Kanda ya Tume ya Ushindani (FCC) - Nyanda ya Juu Kusini, Bw. Dickson Mbanga,akitoa elimu kuhusiana madhara ya bidhaa bandia kwa wanafunzi wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Njombe (FDC) ikiwa ni sehemu ya kuelekea Maadhimisho ya Wiki ya Siku ya Haki za Mlaji Duniani 2026.

  Afisa Mlinda Mlaji kutoka FCC Bw.Anderson Lwiza,akitoa elimu kuhusiana madhara ya bidhaa bandia kwa wanafunzi wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Njombe (FDC) ikiwa ni sehemu ya kuelekea Maadhimisho ya Wiki ya Siku ya Haki za Mlaji Duniani 2026.

  Afisa Mlinda Mlaji kutoka FCC Bw.Anderson Lwiza,akitoa elimu kuhusiana madhara ya bidhaa bandia kwa wanafunzi wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Njombe (FDC) ikiwa ni sehemu ya kuelekea Maadhimisho ya Wiki ya Siku ya Haki za Mlaji Duniani 2026.

Sehemu ya wanafunzi wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Njombe (FDC) Mkoani Njombe wakisikiliza mada mbalimbali wakati wakipata aelimu kuhusiana madhara ya bidhaa bandia yaliyotolewa  na FCC ikiwa ni sehemu ya kuelekea Maadhimisho ya Wiki ya Siku ya Haki za Mlaji Duniani.


Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu Ndugu Bakari Machumu akiwa kwenye picha na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Serikali, Ndugu Gerson Msigwa katika Ofisi ya Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu jijini Dar es Salaam, tarehe 20 Machi, 2026.
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu Ndugu Bakari Machumu akizungumza na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Serikali, Ndugu Gerson Msigwa katika Ofisi ya Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu jijini Dar es Salaam, tarehe 20 Machi, 2026.
▫️Hatua kubwa kwa maendeleo ya Ngumi Kimataifa

20-03-2026 - Dar es Salaam.
SHIRIKISHO la Ngumi Tanzania (BFT) linapenda kuutaarifu umma na wadau wa mchezo wa ngumi kuwa Tanzania imekuwa rasmi mwanachama wa World Boxing, Shirikisho la Kimataifa la Ngumi linalotambuliwa na Kamati ya Olimpiki ya Kimataifa (IOC).

Uamuzi wa kuipokea Tanzania ulifikiwa katika kikao cha Kamati ya Utendaji ya World Boxing kilichofanyika tarehe 15-03-2026, ambapo Tanzania iliungana na mataifa mengine nane yaliyopitishwa kuwa wanachama wapya.

Mataifa hayo ni Zambia, Msumbiji, Urusi, Tonga, Cyprus, Belarus, Niue na Papua New Guinea.

Kwa uamuzi huo, World Boxing sasa ina jumla ya wanachama 168 duniani, hatua inayoendelea kuimarisha ukuaji na usimamizi wa mchezo wa ngumi kimataifa.

World Boxing imepewa dhamana na Kamati ya Olimpiki ya Kimataifa (IOC) kusimamia na kuratibu mashindano ya ngumi katika matukio makubwa ya kimataifa, ikiwemo Michezo ya Olimpiki, Michezo ya Jumuiya ya Madola, pamoja na Michezo ya Kimabara kama African Games.

Akizungumzia mafanikio hayo, Rais wa Shirikisho la Ngumi Tanzania (BFT), Ndg. Lukelo Willilo, amesema:

“Kupatikana kwa uanachama wa World Boxing ni hatua muhimu na ya kihistoria kwa maendeleo ya ngumi nchini Tanzania. Fursa hii itawawezesha mabondia wetu kushiriki kikamilifu katika mashindano ya kimataifa na kuongeza ushindani pamoja na viwango vyao. Tunaendelea kujipanga kuhakikisha Tanzania inanufaika ipasavyo na uanachama huu.”

Kupatikana kwa uanachama huu ni hatua muhimu kwa maendeleo ya mchezo wa ngumi nchini Tanzania, kwani utafungua fursa zaidi kwa mabondia kushiriki mashindano ya kimataifa na kukuza viwango vya ushindani.

 Na MWANDISHI WETU


NAIBU Kadhi Mkuu Sheikh Khamis Ngeruko, amevitaka vituo vya kulea yatima nchini kuto kufuga watoto hao badala yake wawalee na kuwakuza katika maadili mema.

Ameyasema hayo Dar es Salaam katika futari iliyoandaliwa na Kampuni ya Yono Auction Mart katika Kituo cha Kulea Yatima cha Mwana, kilichopo Vingunguti, juzi.

Akizungumza kwa niaba ya Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania Dk. Aboubakar Zubeir, Naibu Kadhi Sheikh Ngeruko, ameeleza vipo vituo vinavyo ishi na yatima kwa mfumo wa kuwafuga hali ambayo haiwakuzi katika njia inayo paswa.

“Yatima anatakiwa kulelewa siyo kufugwa. Alelewe kama mtata anaye lelewa akiwa nyumbani. Apewe mahitaji yote muhimu hususan elimu dunia na elimu ahera kulingana na imani ya mtoto,”alieleza Sheikh Ngeruko.

“Nataka tuandae semina itakayo washirikisha watu wanaoendesha vituo hivi vya kulea watoto. Tuwape elimu hii ya kuto kuwa fuga badala yake wawalee ili baada ya kukua wajitegemee kimaisha na kuwa na maadili mema,”alisema.

Awali Mkurugenzi Mkuu wa Yono Auction Mart, Stanley Kevela, alisema wataendeleza utamaduni wa kusaidia makundi yenye mahitaji maalumu hususan kutoa sadaka kwa yatima kwani hata vitabu vitakatifu vimeelekeza hilo.

Makamu Mkurugenzi Mkuu wa Yono Auction Mart, Dk.Scolastica Kevela, alikemea vikali wanawake wanao tupa watoto baada ya kujifungua na kuitaka jamii kulaani vitendo hivyo.

Dk. Scolastica ambaye ni Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Mkoa wa Njombe, alimpongeza Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kitendo cha kishujaa cha kumwasili mtoto mchanga hivi karibuni.

“Tunamshukuru Rais Dk. Samia kwa kitendo hicho kinacho thibitisha, upendo na kujali malezi ya watoto. Nikiwa mmoja wa wanawake wanao kemea ukatili na toa wito kwa jamii kusimamia malezi ya watoto wetu,”alisema.

Alieleza,kampuni yake itaendelea na utamaduni wa kutoa gawio kwa jamii hususan wenye mahitaji maalumu, kushiriki shughuli za maendeleo kuunga mkono jitihada za Rais Dk. Samia.

“Wito wangu kwa jamii. Kama umeajaaliwa kipato toa kiasi kwa jamii hasa watoto hawa wenye mahitaji maalumu. Mungu atakubariki kwani mali na fedha vyote tutaviacha hapa duniani,”alisema Dk. Kevela.

Uongozi wa Kituo cha Mwana ulishukuru wadau hao kuwakumbuka watoto katika mwezi mtukufu wa Ramadhani na kuomba jamii kuendelea kusaidia kituo hicho chenye watoto 55 wa jinsia na rika mbalimbali.






Na Mwandishi Wetu
MBUNGE wa Jimbo la Mbarali, Bahati Ndingo, amesema ataongoza jimbo hilo kwa kusikiliza wananchi na kuwasemea katika vyombo vya maamuzi ili kutafuta suluhisho la changamoto zinazowakabili.

Akizungumza katika mahojiano na mwandishi, Ndingo alisema katika kipindi chake cha ubunge atakuwa daraja kati ya wananchi na Serikali kwa kuhakikisha maoni, ushauri na mapendekezo yao yanapelekwa kwenye hatua za utekelezaji.

Alisema dhamira yake ni kufuatilia kwa karibu masuala muhimu ya maendeleo ya jimbo hilo, hususan kwa kuibua hoja na kuzifikisha bungeni ili zipatiwe ufumbuzi kwa manufaa ya wananchi wa Mbarali.

“Ubunge wangu huu nitakuwa daraja la wananchi wangu, kuwasikiliza kwa yale wanayonishauri na kuyapeleka katika hatua za utekelezaji huku nikifuatilia zaidi,” alisema Ndingo.

Mbunge huyo alisema Mbarali ni miongoni mwa maeneo yanayotegemea zaidi uchumi wa kilimo, hasa zao la mpunga, hivyo kuna umuhimu mkubwa wa kuboresha miundombinu ya barabara ili kurahisisha usafirishaji na shughuli nyingine za kijamii na kiuchumi.

Alieleza kuwa kipindi cha masika kimesababisha baadhi ya barabara kuharibika, jambo ambalo limeathiri mawasiliano kati ya maeneo mbalimbali ya jimbo hilo. Hata hivyo, alisema matarajio ni kwamba Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) utaanza kazi ya kurekebisha miundombinu hiyo mara baada ya mvua kupungua.

Ndingo pia alisema amejiwekea dhamira ya kutumia nafasi yake katika Bunge lijalo kutoa mchango mkubwa zaidi kwa maendeleo ya wananchi wa Mbarali, kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo.

Aidha, alisema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ina nia ya dhati ya kuwahudumia wananchi, na kwamba yeye kama mbunge anao wajibu wa kuunga mkono jitihada hizo kwa kutoa ushauri na mchango unaolenga kuharakisha maendeleo ya jimbo hilo.

Kwa upande mwingine, aliwataka wananchi wa Mbarali kuwa na umoja na kuzungumza lugha moja yenye lengo la kujenga jimbo lao kwa pamoja, akisisitiza kuwa maendeleo ya kweli yanahitaji mshikamano na ushirikiano kutoka kwa kila mmoja.

Alisema kwa ushirikiano huo, Mbarali inaweza kufikia maendeleo yanayoonekana na kuwanufaisha wananchi wake katika sekta mbalimbali za kiuchumi na kijamii.
Naibu Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile, ametembelea Bandari ya Durban iliyopo nchini Afrika Kusini, kwaajili ya kujionea utendaji na uwekezaji mkubwa katika bandari hiyo inayohesabika miongoni mwa bandari kuu za kontena barani Afrika.

Bandari ya Durban ina jumla ya gati 58 zinazohudumia aina mbalimbali za mizigo ikiwemo makasha (containers), magari, mizigo ya kawaida (break bulk), mizigo mikavu (dry bulk), pamoja na abiria. Kwa mwaka, bandari hiyo hushughulikia makasha milioni 2.6, tani milioni 13 za mizigo mikavu, tani milioni 4.6 za break bulk, magari 560,000 na takribani kilolita milioni 22 za mizigo ya vimiminika (liquid bulk).

Akizungumza baada ya ziara hiyo iliyofanyika Machi 20, 2026, Waziri Kihenzile amesema ameridhishwa na kiwango kikubwa cha uwekezaji katika miundombinu ya bandari na reli, pamoja na namna ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi unavyoongeza ufanisi wa huduma bandarini.

Ametolea mfano mkataba wa miaka 25 kati ya bandari hiyo na kampuni ya ICTSI ulioanza Januari 2026 kwa ajili ya kuendesha Pier 2, unaolenga kuongeza uwezo wa kuhudumia makasha (TEUs) na kuongeza kasi ya utendaji kazi bandarini kwa zaidi ya mara mbili.

Waziri huyo amesema uzoefu huo unaonesha umuhimu wa sekta binafsi katika kuboresha ufanisi wa bandari, ambapo amebainisha kuwa Tanzania tayari inanufaika na ushiriki wa sekta binafsi kupitia kampuni kama DP World na Adani Ports (kupitia TEAGTL/TICTS) katika uendeshaji wa sehemu ya bandari.

Aidha, ameeleza kuwa juhudi hizo zinaenda sambamba na uwekezaji wa Serikali katika miundombinu ya reli, ikiwemo Standard Gauge Railway (SGR), Meter Gauge Railway (MGR) na TAZARA, ili kuharakisha upakiaji, upakuaji na usafirishaji wa mizigo.

Amehitimisha kwa kusema kuwa Bandari ya Dar es Salaam inaendelea kuimarika kila siku na kuwa lango lenye ushindani mkubwa kwa nchi za Afrika Mashariki na Kati, huku ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi ukiendelea kuleta matokeo chanya katika sekta ya uchukuzi.










Tanzania yafanya maandalizi ya kuendesha mafunzo na kongamano la ushirikishwaji wa wanawake kwenye usuluhishi wa migogoro kwa njia mbadala ili kuongeza idadi ya wanawake waliothibitishwa kwenye ngazi ya maamuzi na ushiriki kwenye utatuzi wa migogoro ndani na nje ya nchi.

Hayo yameelezwa leo na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Kituo cha Kimataifa cha Usuluhishi Tanzania (Tanzania International Arbitration Centre – TIAC), ndugu Godson Nyange wakakti akizungumza na waandishi wa habari kwenye ukumbu wa Wakili House, Dar es Salaam ili kuhabarisha umma kuhusu matukio hayo ambayo yamepangwa kufanyika tarehe 24 hadi 27 Machi, 2026 jijini Dar es Salaam

Ndugu Nyange amesema kuwa kongamano hilo litafanyika tarehe 27 Machi, 2026 na litaongozwa na kauli mbiu isemayo, “Kutoka Majadiliano hadi Hatua: Kuendeleza Ushirikishwaji wa Wanawake katika Utatuzi wa Migogoro kwa Njia Mbadala (“From Dialogue to Action: Advancing Women’s Inclusion in Alternative Dispute Resolution (ADR).”) Kongamano hilo litafanyika kwenye ukumbi wa Wakili House jijini Dar es Salaam na litawaleta pamoja wataalamu wa sheria, watunga sera, wanataaluma, viongozi wa biashara, wataalamu wa ADR pamoja na wataalamu kutoka kada mbalimbali ili kuzitathimini kwa kina hatua za kuongeza ushiriki wa wanawake katika utatuzi wa migogoro.

Pia, ameongeza kuwa kongamano hilo litatanguliwa na mafunzo yatakayofanyika tarehe 24 hadi 26 Machi, 2026 na yatafanyika kwenye ukumbi wa Wakili House jijini Dar es Saalam ambapo mafunzo hayo yataongozwa na mada isemayo, “Kujenga Uwezo na Kujiamini kwa Wanawake katika Utatuzi Mbadala wa Migogoro (ADR).”

“Kihistoria, Sekta ya Utatuzi wa Migogoro kwa Njia Mbadala (ADR) imekuwa ikitawaliwa zaidi na wanaume, huku wanawake wakiwa wachache katika nafasi za usuluhishi (arbitration), upatanishi (mediation) na majukumu mengine ya ADR hasa katika nafasi za juu za kufanya maamuzi. Hali hii imeonekana duniani kote na barani Afrika ambapo tafiti zinaonyesha kuwa takribani asilimia 72 ya wasuluhishi katika kesi zinazohusiana na Afrika ni wanaume, wakati asilimia 28 tu ni wanawake. Vilevile, wanawake wanawakilisha takribani asilimia 29 hadi 34 ya uteuzi wa wasuluhishi katika taasisi kubwa za kimataifa za usuluhishi,” amefafanua ndugu Nyange.

Akizungumza kwa niaba ya Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali (OWMS), Bi. Mercy Kyamba, Mkurugenzi Msaidizi – Sehemu ya Udhibiti Ubora wa Ofisi hiyo amesema kuwa OWMS inashirikiana na TIAC kuendesha mafunzo na kufanya kongamano hilo kwa kuwa OWMS pamoja na majukumu mengine, imekasimiwa na kupewa dhamana ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kusimamia na kuendesha mashauri ya usuluhishi ndani na nje ya nchi kwa niaba ya Serikali.

Bi. Kyamba amesema kuwa uwepo wa mafunzo hayo na kongamano hilo ni dhamira ya pamoja ya TIAC na OWMS ya kuimarisha nafasi ya wanawake katika usuluhishi (arbitration), upatanishi (mediation) na mifumo mingine ya ADR. Mafunzo hayo yataendeshwa na wataalam wabobezi wa ndani na nje ya nchi na yamelenga kuwapatia wanawake maarifa, ujuzi wa vitendo na kujiamini kunakohitajika ili kushiriki kikamilifu katika michakato ya ADR.

Pia, Bi. Kyamba ameongeza kuwa maeneo muhimu yatajadiliwa kwenye mafunzo hayo yanahusu misingi ya usuluhishi (arbitration) na upatanishi (mediation); ujuzi wa vitendo katika majadiliano na usimamizi wa migogoro; viwango vya maadili na wajibu wa kitaaluma katika ADR; njia za kujenga taaluma na kupata ithibati katika ADR; na mikakati ya kujenga kujiamini na uwepo wa kitaaluma katika mashauri ya utatuzi wa migogoro.

Aidha, amesema kuwa kwa upande wa Kongamano, linatarajiwa kuwa jukwaa la kiwango cha juu la kujadili namna ya kuongeza ushiriki wa wanawake katika ADR ambapo majadiliano ya jopo la wataalamu yatawakutanisha wadau mashuhuri ili kuchambua masuala muhimu yakiwemo nafasi ya wanawake katika kuimarisha mifumo ya ADR; msaada wa taasisi katika kukuza wanawake katika usuluhishi na upatanishi; kujenga mitandao ya kitaaluma na fursa za ulezi (mentorship) kwa wataalamu wapya wa ADR; na athari pana ya utofauti wa kijinsia katika utoaji haki na imani ya kibiashara.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa TIAC, Bi, Magreth Magoma amesema kuwa mafunzo na kongamano hilo ni sehemu ya juhudi pana za TIAC za kukuza matumizi na maendeleo ya utatuzi mbadala wa migogoro nchini Tanzania na katika ukanda mzima wa Afrika Mashariki na kutachangia katika kujenga mfumo madhubuti na unaoaminika wa utatuzi wa migogoro unaosaidia upatikanaji wa haki, uhakika wa biashara na kuimarisha uwekezaji.

Bi. Magoma ameongeza kuwa kupitia uwepo wa Sheria ya Usuluhishi nchini ya mwaka 2020 ambayo inaelekeza kuwa mtu yeyote anayetaka kufanya usuluhishi lazima apate ithibati kutoka Wizara ya Katiba na Sheria. “Sheria hii ilianza utekelezaji wake mwaka 2021 ambapo hadi sasa Wizara imewapatia ithibati na kuwathibitisha jumla ya wanaume 444 katika eneo la usuluhishi na wanawake 89; majadiliano wanaume 162 na wanawake 38; wapatanishi wanaume 142 na wanawake 56; na upatanishi wanaume 77 na wanawake 14,” amefafanua Bi. Magoma.

Mafunzo na kongamano hilo litaangazia umuhimu wa uwiano wa kijinsia katika utatuzi wa migogoro, kujadili mikakati ya kuongeza uelewa na ushiriki na uongozi wa wanawake katika ADR ili kuwawezesha wanawake katika ADR na kuimarisha taaluma zao, kuchangia mfumo wa utatuzi wa migogoro ulio na uwiano, unaojumuisha wadau wote na unaoaminika zaidi.
Ndugu Godson Nyange, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Kituo cha Kimataifa cha Usuluhishi Tanzania (TIAC) akiongea na waandishi wa habari kuhusu mafunzo na kongamano la ushirikishwaji wa wanawake kwenye utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala yanayotarajiwa kufanyika tarehe 24 hadi 27 Machi, 2026 Jijini Dar es Salaam.

Bi. Mercy Kyamba, Mkurugenzi Msaidizi Sehemu ya Udhibiti Ubora wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali akizungumzia ushirikiano uliopo kati ya Ofisi hiyo na Kituo cha Kimataifa cha Usuluhishi Tanzania wakati wa mkutano na waandishi wa habari kuhusu mafunzo na kongamano la ushirikishwaji wa wanawake kwenye utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala yanayotarajiwa kufanyika tarehe 24 hadi 27 Machi, 2026 Jijini Dar es Salaam.
Bi. Magreth Magoma, Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Kimataifa cha Usuluhishi Tanzania (TIAC) akitoa ufafanuzi kwa waandishi wa habari kuhusu mafunzo na kongamano la ushirikishwaji wa wanawake kwenye utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala yanayotarajiwa kufanyika tarehe 24 hadi 27 Machi, 2026 Jijini Dar es Salaam.




Watumishi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali na Kituo cha Kimataifa cha Usuluhishi Tanzania (TIAC) wakimsikiliza ndugu Godson Nyange (hayupo pichani) Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Kituo cha Kimataifa cha Usuluhishi Tanzania wakati akiongea na waandishi wa habari kuhusu mafunzo na kongamano la ushirikishwaji wa wanawake kwenye utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala yanayotarajiwa kufanyika tarehe 24 hadi 27 Machi, 2026 Jijini Dar es Salaam.


-WAZIRI DKT. GWAJIMA KUANZISHA JUKWAA LA MAJADILIANO ENDELEVU YA KISEKTA KUHUSU MIKUTANO YA WIZARA KIMATAIFA.

Na WMJJWM New York Marekani

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima amesema, Serikali kupitia Wizara anayoiongoza itaanzisha Jukwaa endelevu la majadiliano ya Kisekta litakaosaidia kuongeza ufanisi wa ushiriki wa Nchi katika Mikutano ya kimataifa inayogusa maendeleo ya Wanawake na Jinsia.

Waziri Dkt. Gwajima ameyasema hayo jijini New York nchini Marekani mara baada ya kuhitimishwa kwa Mkutano wa 70 wa Hali ya Wanawake Duniani (CSW 70) ambapo, Tanzania ilishiriki na kueleza mafanikio iliyopata katika kuhakikisha upatikanaji wa haki kwa wanawake na wasichana.

Waziri Dkt. Gwajima amesema jukwaa hilo litasaidia kuwepo kwa uelewe wa pamoja kati ya Serikali na wadau wengine wote katika kuratibu ushiriki wa nchi katika mikutano mbalimbali ya kimataifa hasa inayogusa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum ili kuongeza ufanisi zaidi.

“Ni muhimu tuwe na Jukwaa hili ambalo litasaidia kuturatibu Serikali na wadau wetu wote ili, tunapotaka kushiriki katika Mikutano ya Kimataifa tuwe na uelewa wa pamoja na maandalizi ya pamoja ya kwenda kuitangaza nchi kimataifa” amesisitiza Waziri Dkt. Gwajima

Ameeleza kuwa, Tanzania imeshiriki mikutano mbalimbali iliyoandaa na iliyoalikwa ikiwa na lengo la kueleza mafanikio ya nchi katika suala la upatikanaji wa haki kwa wanawake na watoto wa kike na pia kujifunza namna mataifa mengine wanavyotekeleza suala hilo.

Aidha ameongeza kuwa, taarifa ya ushiriki wa Nchi katika Mkutano wa 70 wa Hali ya Wanawake Duniani itatolewa mara baada ya ujumbe ulioshiriki Mkutano huo kuwasili nchini.

Mkutano huo uliofunguliwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres Machi 09, 2026 uliongozwa na Kaulimbiu isemayo "Kuhakikisha na Kuimarisha upatikanaji wa Haki kwa Wanawake na Wasichana wote, ikiwa ni pamoja na kukuza mifumo ya kisheria nyenye usawa na jumuishi, kuondoa sheria, sera, na desturi za kibaguzi na kushughulikia vikwazo vya kimuundo", (Ensuring and Strengthening access to justice for all Women and Girls, including by promoting inclusive and equitable legal system, eliminating discriminatory laws, policies, and practices and addressing structural barriers”).











Top News