📍Ampongeza Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuboresha barabara nchini


Na Mwandishi Wetu, Mbeya.

SERIKALI imewagiza mameneja na wahandisi wa TANROADS na TARURA nchini kutumia mifumo mipya ya kielektroniki kulinda hifadhi za barabara na kutekeleza miradi kwa viwango.

Agizo hilo limetolewa Jijini Mbeya Leo Juni 17 2026 na Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Mhe. Solomon Itunda, wakati akimwakilisha Mkuu wa Mkoa huo, Mhe. Beno Malisa, kufungua mafunzo ya viongozi wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) na Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA).

Mafunzo hayo ya siku nne yaliyoanza Jumatatu, Juni 15, 2026, yamewakutanisha Mameneja, Wahasibu, na Wahandisi kutoka mikoa ya kimkakati ya kiuchumi ikiwemo Mbeya, Songwe, Rukwa, Ruvuma, Mtwara, na Lindi.

Teknolojia na Udhibiti wa Miundombinu

Mhe. Itunda amebainisha kuwa lengo kuu la semina hiyo ni kuwajengea uwezo viongozi hao katika kusimamia miradi ya miundombinu kwa ufanisi, hasa kupitia matumizi ya mfumo mpya wa kielektroniki unaodhibiti na kusimamia matumizi holela ya hifadhi za barabara nchini.

Alitumia jukwaa hilo kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kumwaga mabilioni ya fedha katika ujenzi wa barabara, hatua iliyoleta mageuzi makubwa ya kijamii na kiuchumi.

"Serikali inaendelea kuhakikisha kuwa barabara zinajengwa na kuboreshwa ili kufungua fursa za kiuchumi kwa wananchi. Tunampongeza Mheshimiwa Rais Samia kwa juhudi hizi kubwa, na nitoe wito kwenu washiriki kutumia mafunzo haya kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yenu," alisisitiza Mhe. Itunda.


Mapinduzi ya Kiuchumi vijijini

Pia, DC Itunda amewahimiza washiriki kutumia ipasavyo maarifa hayo ya kidijitali kuhakikisha utekelezaji wa miradi unazingatia viwango na taratibu zilizowekwa kiofisi bila kuwa na changamoto zozote.

Kitalamu, mafunzo haya yanatarajiwa kuwa chachu ya kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi hizo mbili (TANROADS na TARURA), kuongeza uwajibikaji, na kurahisisha usafirishaji wa bidhaa za kilimo na biashara katika ukanda wa Nyanda za Juu Kusini na taifa kwa ujumla.







Na Clement Robert, WAF - Dodoma

Tanzania imeeleza utayari wake wa kuunga mkono juhudi za kukabiliana na mlipuko wa ugonjwa wa Ebola unaoendelea katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na Uganda kwa kutoa vifaa tiba, vifaa kinga kwa wahudumu wa afya pamoja na wataalamu wenye uzoefu katika kudhibiti milipuko ya magonjwa.

Kauli hiyo imetolewa leo Juni 16,2026 na Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, wakati wa Mkutano wa Ngazi ya Juu wa Wakuu wa Nchi na Serikali pamoja na wadau uliojadili hatua za kukabiliana na mlipuko wa virusi vya Ebola aina ya Bundibugyo katika nchi hizo mbili.

Amesema, Tanzania imeeleza mshikamano wake na serikali pamoja na wananchi wa DRC na Uganda, huku ikitoa pole kwa familia zilizopoteza wapendwa wao kutokana na ugonjwa huo na kuwatakia nafuu ya haraka wagonjwa wote walioathirika.

“Tanzania tumeendelea kuimarisha uwezo wa kujiandaa na kukabiliana na milipuko ya magonjwa kupitia uwekezaji katika mifumo ya ufuatiliaji wa magonjwa, uchunguzi katika maeneo ya mipakani, maabara, vifaa tiba na mifumo ya mwitikio wa haraka, huku tukijidhatiti na kujna umuhimu wa ushirikiano wa kikanda na bara zima”

Mhe. Mchengerwa ameongeza, kwa kuitaka Africa CDC pamoja na nchi wanachama kuimarisha zaidi uratibu, kuwekeza katika mifumo ya maandalizi na mwitikio wa haraka, na kuhakikisha rasilimali zinapatikana kwa wakati ili kudhibiti mlipuko wa sasa, kuzuia majanga yajayo na kujenga Afrika yenye afya na usalama zaidi.

 Aidha, Tanzania imepongeza juhudi za Rais wa Burundi, Mheshimiwa Ndayishimiye, Tume ya Umoja wa Afrika, Kituo cha Afrika cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa (Africa CDC) na Shirika la Afya Duniani (WHO) kwa uratibu na uongozi wao katika kuitisha mkutano huo na kusimamia hatua za mwitikio dhidi ya mlipuko huo.





Airtel Tanzania imezindua minara miwili mipya ya mawasiliano ya 4G inayotumia umeme wa gridi ya taifa katika mikoa ya Geita na Dodoma, hatua inayotarajiwa kuboresha upatikanaji wa simu na intaneti kwa maelfu ya wananchi wa maeneo ambayo kwa muda mrefu yamekosa mawasiliano ya uhakika.

Minara hiyo imejengwa katika Kata ya Nyaruyeye, Wilaya ya Geita, na Kijiji cha Chinagali, Kata ya Zoissa, Wilaya ya Kongwa, Mkoa wa Dodoma, ikiwa na lengo la kuboresha mawasiliano, huduma za intaneti na huduma za kifedha kupitia simu kwa jamii zilizokuwa zikikabiliwa na changamoto za mtandao kwa miaka mingi.

Tofauti na minara mingine ya vijijini inayotegemea majenereta, minara hiyo imeunganishwa na umeme wa gridi ya taifa huku ikiwa na majenereta ya akiba, hatua inayopunguza gharama za uendeshaji na kuchangia uhifadhi wa mazingira kupitia kupunguza matumizi ya mafuta.

Katika Kata ya Nyaruyeye, zaidi ya wananchi 15,000 pamoja na wakazi wa Kata ya Nyarugusu na maeneo jirani wanatarajiwa kunufaika na maboresho hayo.

Uwekezaji huo unafuatia tathmini iliyofanywa na Airtel baada ya kupokea malalamiko ya wananchi kuhusu changamoto za upatikanaji wa huduma za mawasiliano katika maeneo hayo.

Hatua hiyo inalenga kuimarisha mawasiliano, kuongeza ujumuishaji wa kifedha na kufungua fursa za kidijitali kwa jamii.

Viongozi wa maeneo husika wamesema minara hiyo itasaidia shughuli za elimu, biashara na utoaji wa huduma za umma, pamoja na kuchochea shughuli za kiuchumi, hususan katika maeneo yanayojishughulisha na kilimo na ufugaji kama Wilaya ya Kongwa.

Airtel imesema uwekezaji huo ni sehemu ya mkakati wake wa kuhakikisha wananchi wa vijijini wanapata fursa sawa katika uchumi wa kidijitali kupitia upatikanaji wa miundombinu ya mawasiliano ya uhakika





Na Karama Kenyunko, Michuzi TV

MSIMAMIZI wa tanki la mafuta ghafi, Kassim Kongwa na wenzake sita wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa kesi ya Uhujumu yenye mashtaka matatu, limo la wizi wa lita 2,800 za mafuta ya ghafi mali ya kampuni ya Mikoani Edible Oil and Detergents Limited.

Katika hati ya mashtaka iliyosomwa mahakamani hapo leo Juni 16, 2026 na wakili wa serikali Winiwa Kasala imewataja washtakiwa wengine kuwa ni Hassan Kimoge, Juma Issah, Halfan Halfan maarufu kama Ruba, Maria Gulaba wote ni ma opereta wa kiwanda hicho, Hemed Abdalah kibarua wa Kampuni ya Azania na mlinzi Jafar Molel.

Mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu Anna Magutu imedaiwa kati ya Juni 2 na 4, 2026 jijini Dar es Salaam, washtakiwa wakiwa na nia ovu waliongoza genge la uharifu na kuiba mafuta ghafi mali ya kampuni ya Mkoani Edible Oil and Detergents Ltd.

Imeendelea kudaiwa kuwa katika tarehe hizo huko Temeke katika mtaa wa Moringe, Wilaya ya Temeke, washtakiwa waliiba lita 2800 za mafuta ghafi yenye thamani ya sh milioni 26, mali ya kampuni hiyo.

Aidha katika shtaka la utakatishaji washtakiwa hao wanadaiwa kujipatia kiasi lita 2800 za mafuta huku wakijua kuwa mafuta hayo nu zao la kosa tangulizi la wizi.

Hata hivyo washtakiwa hao hawakuruhusiwa kujibu chochote mahakamani hapo kwa kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo ya Uhujumu Uchumi ambazo kwa kawaida kusikilizwa mahakama Kuu au kwa kibali maalumu kutoka kwa DPP

Kwa mujibu wa upande wa mashtaka upelelezi katika kesi hiyo bado haujakamilika. Kesi imeahirishwa hadi Juni 30,2026 itakapotajwa tena, washtakiwa wote wamepelekwa mahabusu kwasababu shtaka la utakatishaji fedha halina dhamana.





Meneja wa Huduma za Jamii na Matuko wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Abigail Lukuvi (wa pili kutoka kushoto), akikabidhi vifaa vya hospitali kwa Muuguzi Kiongozi wa Hospitali ya Mnazi Mmoja, Bi. Shufaa Kaniki (kulia), katika hafla iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana. Kushoto ni Makamu wa Rais wa The Runners Club, Bw. Godfrey Mwangungulu, pamoja na baadhi ya wafanyakazi wa hospitali. Utoaji huu wa vifaa, wenye lengo la kuimarisha huduma za afya ya mama na mtoto, umefuatia mafanikio ya mbio za Absa Dar City Marathon zilizofanyika tarehe 3 Mei 2026 jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya wafanyakazi wa Hospitali ya Mnazi Mmoja wakionesha vifaa vipya vya hospitali walivyokabidhiwa na Meneja Huduma za Jamii na Matukio wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Abigail Lukuvi (kushoto), katika hafla iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana. Utoaji huu, wenye dhamira ya kuimarisha huduma za afya ya mama na mtoto, umewezekana kufuatia mafanikio ya mbio za Absa Dar City Marathon zilizofanyika tarehe 3 Mei 2026, jijini Dar es Salaam.

Makamu wa Rais wa The Runners Club, Bw. Godfrey Mwangungulu, akitoa hotuba yake wakati wa hafla ya makabidhiano ya vifaa vya hospitali vilivyotolewa na Benki ya Absa Tanzania jijini Dar es Salaam jana. Mchango huu Kutoka Benki ya Absa, wenye lengo la kuunga mkono huduma za afya ya mama na mtoto, umewezekana kufuatia mafanikio ya mbio za Absa Dar City Marathon zilizofanyika tarehe 3 Mei 2026 jijini Dar es Salaam.
 Muuguzi Kiongozi wa Hospitali ya Mnazi Mmoja, Bi. Shufaa Kaniki, akitoa shukrani zake baada ya kupokea msaada wa vifaa vya hospitali kutoka kwa Meneja Huduma za Jamii na Matukio wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Abigail Lukuvi (kushoto), katika hafla iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana. Utoaji huu, unaolenga kuimarisha huduma za afya ya mama na mtoto, umefuatia mafanikio ya mbio za Absa Dar City Marathon zilizofanyika tarehe 3 Mei 2026 jijini Dar es Salaam.
Na Victor Masangu,Kibaha

Mwenyekiti wa umoja wa wanawake (UWT) Mkoa wa Pwani Zainabu Vullu amewahimiza wanawake kuweka misingi imara ya kutumia fursa za mikopo ya asilimia 10 ambayo inatolewa na Hamashauri kwa lengo la kuweza kujikwamua kiuchumi na kuondokana na wimbi la umasikini.

Vullu ameyabainisha hayo wakati wa ziara yake ya kikazi katika Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha ambapo ameweza kutembelea katiika kata mbili za Tumbi pamoja na Kata ya Kongowe ambapo ameambatana na kamati ya utekelezaji ya Mkoa pamoja na vingozi ngazi ya Wilaya.

Katika ziara hiyo Mwenyekiti huyo ameweza kupata fursa ya kutembelea baadhi ya miradi ikiwemo katika sekta ya elimu ambapo ameweza kutembelea na kukagua mradi wa ujenzi wa choo salama katika wa sekondari ya Kibaha pamoja na kituo cha afya Kongowe.

Mwenyekiti huyo amesema kwamba lengo kubwa la kufanya ziara hiyo ni kwa ajili ya kuwashukuru umoja wa wanawake UWT kwa kuweza kuwa pamoja na mshikamano wa kukiwezesha chama cha mapinduzi kuweza kushinda kwa kishindo katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2025 na kuwapoitisha viongozi katika ngazi mbali mbali ikiwemo udiwani, Ubunge pamoja na nafasi ya Urais.

Naye Katibu wa UWT Wilaya ya Kibaha mjni Cesilian Ndaru amesema kwamba lengo lako kubwa ni kuhakikisha wanaweka mikakati madhubuti ya kuwa na vitega uchumi ambavyo vutaweza kuwasaidia kwa kiasi kikubwa katika kijikwamua kiuchumi.

Katibu Ndaru amebainisha kwamba umoja huo wameweka mipango madhubuti ya kuwa na miradi mbali mbali ya maendeleo ikiwemo kuanzisha miradii ya kuwa na nyumba za makatibu kila kata kwa ajili ya kuwawezesha makatibu kuwa na sehemu na makazi ya kusihi ili kuweza kufanya kazi zao kwa ufanisi.

Naye mlezi wa UWT Wilaya ya Kibaha mjini Mama Selina Koka ambaye pia ni mke wa Mbunge wa Jimbo la Kibaha mjini amesema kwamba ataendelea kushirikiana bega kwa bega na wanawake katika kuhakikisha kwamba wanaimarisha jumuiya hiyo.

Mama Koka amebainisha kwamba lengo lake kubwa ni kuendelea kushirikiana kwa pamoja na viongozi wenzake katika kufanya kazi kwa bidii na kumuunga mkono Rais wa awamu ya sita Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuleta chanchu ya maendfeleo ikiwa pamoja na kuwainua kiuchumi wanawake wenzake.

Ziara ya Mwenyekiti wa UWT Mkoa wa Pwani imefanyika katika Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha ambapo ameweza kupata fursa ya kutembnelea baadhi ya mikradi ya maendeleo ikiwemo katika shule ya sekondari ya wasichana Kibaha pamoja na kituo cha afya Kongowe ikiwa pamoja na kuzungumza na wanawake wa umoja huo.




Serikali za Mitaa kwa kushirikiana na wazazi na walezi mkoani Geita wametakiwa kuthamini na kulinda haki za watoto kwa kuwakinga dhidi ya ukatili na unyanyapaa.

Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Geita, Mhe. Hashim Komba, aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Geita katika maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika. Maadhimisho hayo ya kimkoa yamefanyika katika Kata ya Nyawilimilwa, Wilaya ya Geita.

Mhe. Komba amesema Serikali haitaona aibu kuwachukulia hatua za kisheria wazazi au walezi wanaowanyima watoto wao haki ya msingi ya kupata elimu na haki nyingine zilizowekwa na sheria za nchi. Amesema ulinzi wa mtoto ni wajibu wa kila mzazi na jamii kwa ujumla.

Akitoa taarifa ya utekelezaji, Ofisa Ustawi wa Jamii Mkoa wa Geita, Bw. Frank Moshi, ameeleza mafanikio yaliyopatikana pamoja na mikakati inayoendelea kutekelezwa ili kudhibiti vitendo vya ukatili na uhalifu unaofanywa dhidi ya watoto mkoani humo. Amesema jitihada hizo zimeleta matumaini kwa watoto wengi waliokuwa katika mazingira hatarishi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la NELICO linalojihusisha na utetezi na ulinzi wa haki za watoto mkoani Geita, Bi. Paulina Alex Majogoro, amesema shirika hilo linaendelea kutoa msaada kwa watoto. Msaada huo ni pamoja na ushauri wa kisheria, sare za shule na mahitaji mengine muhimu kwa familia zenye kipato duni.

Maadhimisho ya mwaka huu yamebeba kaulimbiu ya kuhimiza jamii kutoa kipaumbele kwa ustawi na usalama wa mtoto ili kujenga taifa lenye vizazi vijavyo vyenye maadili na elimu.




Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma

Serikali imeonyesha utayari wa kuangalia uwezekano wa mashindano ya Ligi ya Muungano kuanza kuchezwa pia Tanzania Bara, hatua inayolenga kuimarisha ushiriki wa pande zote mbili za Muungano na kukuza maendeleo ya michezo nchini.

Hoja hiyo iliibuliwa bungeni leo na Mbunge wa Jimbo la Mlalo, Rashid Shangazi, ambaye alihoji sababu za mashindano hayo kuendelea kufanyika Zanzibar pekee kwa muda mrefu na kusisitiza umuhimu wa kuyapanua ili yajumuishe Tanzania Bara.

Akichangia mjadala huo, Shangazi alisema kuwa kuchezwa kwa mashindano hayo katika pande zote za Muungano kutasaidia kuimarisha mshikamano wa kitaifa, kuongeza ushindani wa michezo na kutoa fursa sawa kwa wanamichezo wa Bara na Visiwani.

Akijibu hoja hiyo kwa niaba ya Serikali, Naibu Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Hamisi Mwinjuma, alisema hakuna sheria wala kanuni inayozuia Ligi ya Muungano kuchezwa Tanzania Bara, bali hali iliyopo kwa sasa ni matokeo ya mazoea yaliyojengeka kwa miaka mingi.

Mwinjuma alieleza kuwa suala hilo linaweza kujadiliwa na kufanyiwa maboresho kupitia mazungumzo na makubaliano ya wadau husika ili kuhakikisha mashindano hayo yanawanufaisha wananchi wa pande zote za Muungano.

“Serikali ipo tayari kuendelea kushirikiana na wadau wa michezo kujadili uwezekano wa mashindano haya kufanyika pia Tanzania Bara endapo kutakuwa na makubaliano ya pamoja,” alisema.

Aidha, alibainisha kuwa moja ya sababu zilizochangia mashindano hayo kufanyika zaidi Zanzibar ni kutokana na ukweli kwamba Tanzania Bara tayari ina idadi kubwa ya ligi na mashindano mbalimbali ya soka, hivyo Zanzibar imekuwa ikipewa nafasi ya kuwa mwenyeji wa matukio hayo ili kuongeza shughuli za michezo visiwani.

Hatua hiyo ya Serikali imepokelewa kama ishara ya kufungua ukurasa mpya katika uendeshaji wa Ligi ya Muungano, huku wadau wa michezo wakitarajia kuona mashindano hayo yakipanuliwa zaidi ili kuleta usawa wa ushiriki na kuongeza chachu ya maendeleo ya soka katika pande zote za Muungano.





Na Mwandishi Wetu

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imeanza kushiriki katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma mwaka 2026 yaliyoanza rasmi leo, tarehe 16 mpaka 23 Juni, yanayofanyika katika Viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma

Akizungumza kuhusu ushiriki wa EWURA katika maonesho hayo, Mkurugenzi wa Rasilimali Watu na Utawala wa EWURA, Bi. Hawa Ramadhan Mniga, amesema maonesho hayo ni fursa muhimu kwa Mamlaka hiyo kuwafikia Watanzania na kuwapatia uelewa kuhusu majukumu yake katika usimamizi wa sekta za nishati na maji.

“Wananchi watakaotembelea banda la EWURA watapata fursa ya kujifunza masuala mbalimbali ikiwemo mifumo mbalimbali ya kidijitali inayotumiwa na Mamlaka katika utoaji wa huduma kwa wateja, pamoja na maboresho yanayoendelea kufanyika kwa lengo la kuongeza ufanisi, kasi na ubora wa utoaji wa huduma,” amesema Bi. Mniga.

Ameongeza kuwa eneo lingine lililopatiwa kipaumbele ni uhamasishaji wa matumizi ya nishati safi ya kupikia, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kufanikisha lengo la Taifa la kuhakikisha asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.

Aidha, ametoa rai kwa wananchi, wadau wa sekta mbalimbali na washiriki wa maonesho hayo kutembelea banda la EWURA ili kupata elimu, kuuliza maswali na kufahamu kwa undani huduma zinazotolewa na Mamlaka hiyo.
   


Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu wa benki ya NMB, Ruth Zaipuna (katikati), akiwa na Menejimenti Kuu ya benki hiyo wakionyesha ishara ya furaha mara baada ya uzinduzi wa NMB Mkononi Super App jijini Dar es Salaam, Jumanne, Juni 16, 2026.

Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya NMB, Ruth Zaipuna (kushoto), akijaribu huduma za NMB Mkononi Super App wakati wa uzinduzi wake jijini Dar es Salaam, Jumanne, Juni 16, 2026. Anayemwelekeza kwa kutumia iPad ni Mtaalamu wa Bima wa NMB, Sangwani Mkandawile (katikati).

Mfumo Mpya Waunganisha Mikopo, Bima, Uwekezaji na Huduma za Vikundi

Benki ya NMB imezindua rasmi NMB Mkononi Super App, jukwaa jipya la kidijitali linalounganisha huduma mbalimbali za kifedha katika mfumo mmoja, hatua inayolenga kurahisisha upatikanaji wa huduma za benki na kuimarisha ujumuishaji wa kifedha nchini.

Kupitia jukwaa hilo, wateja wataweza kupata huduma za mikopo, bima, uwekezaji, malipo, huduma za vikundi pamoja na ununuzi wa bando la mawasiliano bila ulazima wa kutembelea matawi ya benki kwa huduma za kawaida.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu wa NMB Bank Plc, Ruth Zaipuna, alisema kuwa NMB Mkononi Super App ni zaidi ya programu ya kibenki, bali ni jukwaa la fursa na uwezeshaji linalolenga kuwahudumia makundi mbalimbali ya Watanzania.

“Jukwaa hili limeundwa kuwawezesha wanafunzi, wafanyakazi, wakulima, wafanyabiashara, wajasiriamali na wawekezaji kusimamia mahitaji yao ya kifedha kwa urahisi kupitia simu zao za mkononi,” alisema Zaipuna.

Katika hatua ya kuongeza upatikanaji wa mitaji, NMB imesema wateja binafsi wanaokidhi vigezo wataweza kuomba mikopo ya hadi Shilingi milioni mbili kupitia programu hiyo, huku wafanyabiashara wadogo wanaostahili wakipata mikopo ya hadi Shilingi milioni tano.

Hata hivyo, wataalamu wa sekta ya fedha wanaona kuwa ongezeko la upatikanaji wa mikopo kidijitali linaifanya elimu ya fedha kuwa muhimu zaidi, hasa katika kuwawezesha wananchi kuelewa gharama za mikopo, masharti ya mikataba, muda wa marejesho na uwezo wao wa kulipa kabla ya kukopa.

Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Ubunifu wa NMB, Josina Njambi, alisema ufunguaji wa akaunti kupitia NMB Mkononi Super App umeboreshwa kwa kiwango kikubwa, ambapo mteja anaweza kufungua akaunti kwa kutumia namba ya simu na namba ya NIDA ndani ya dakika tano pekee.

Alibainisha kuwa mafanikio ya jukwaa hilo hayatategemea tu upana wa huduma zake, bali pia uwezo wake wa kuwasaidia wateja kufanya maamuzi sahihi ya kifedha, kuongeza utamaduni wa kuweka akiba na kutumia huduma za kifedha kwa uwajibikaji.

Uzinduzi wa NMB Mkononi Super App unaashiria hatua nyingine muhimu katika safari ya mageuzi ya kidijitali ya sekta ya benki nchini Tanzania, huku ukionyesha namna teknolojia inavyoendelea kubadilisha upatikanaji na matumizi ya huduma za kifedha kwa wananchi wa kada mbalimbali.

Mkononi Patamu.









Na Mwandishi Wetu.
 
Wabunge wameipongeza Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) kwa kuendelea kupanua wigo wa huduma za hifadhi ya jamii kupitia Skimu ya Hifadhi kwa Wananchi Waliojiajiri, wakisema mpango huo unatoa fursa kwa mamilioni ya Watanzania kunufaika na huduma za hifadhi ya jamii.

Aidha, wamepongeza uwekezaji uliofanywa na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) katika Kiwanda cha Kimataifa cha Bidhaa za Ngozi cha Kilimanjaro (KLICL), wakisema mradi huo una mchango mkubwa katika kukuza viwanda, kuongeza thamani ya mazao ya mifugo na kutengeneza ajira.

Pongezi hizo zilitolewa jijini Dodoma wakati wa semina ya wabunge kuhusu Skimu ya Hifadhi kwa Wananchi Waliojiajiri na Mradi wa Kiwanda cha Kimataifa cha Bidhaa za Ngozi cha Kilimanjaro.

Akizungumza kwa niaba ya Spika wa Bunge, Mhe. Mussa Azzan Zungu, Naibu Spika wa Bunge, Mhe. Daniel Sillo, aliipongeza NSSF pamoja na PSSSF kwa kuendelea kutoa elimu kwa wabunge kuhusu masuala ya hifadhi ya jamii na miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa na mifuko hiyo.

Mhe. Sillo alisema elimu hiyo ni muhimu kwa wabunge kwani itawawezesha kuwa mabalozi wa kuhamasisha wananchi katika majimbo yao kujiunga na mifumo ya hifadhi ya jamii na kufahamu uwekezaji unaofanywa na mifuko hiyo.

Baadhi ya wabunge walioshiriki semina hiyo, akiwemo Mhe. Said Salimu na Mhe. Rashid Shangazi, waliipongeza NSSF kwa juhudi zake za kuwafikia wananchi waliojiajiri na kuimarisha huduma za hifadhi ya jamii nchini.

Walisema skimu hiyo itasaidia kujenga utamaduni wa kuweka akiba, kuongeza usalama wa kipato na kuwapa wananchi waliojiajiri fursa ya kunufaika na huduma za hifadhi ya jamii.

Kwa upande wa uwekezaji wa PSSSF, wabunge Jackson Kiswaga na Rashid Shangazi waliipongeza PSSSF kwa uwekezaji kwenye kiwanda hicho, huku wakiishauri sekta binafsi ikaribushwe katika uendeshaji wa kiwanda ili kuongeza nguvu katika masoko na uzalishaji.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu, alisema Serikali inaendelea kuimarisha huduma za hifadhi ya jamii kwa kuwajumuisha wananchi waliojiajiri, ambao kwa muda mrefu walikuwa nje ya mifumo rasmi ya hifadhi ya jamii licha ya mchango wao mkubwa katika uchumi wa taifa.

Kuhusu PSSSF, Mhe. Sangu alisema mradi wa kiwanda hicho unamilikiwa kwa ubia kati ya Mfuko huo na Jeshi la Magereza kupitia kampuni yake ya Prisons Corporation Sole (PCS) na kuwa umekuwa na manufaa makubwa kwa jamii na taifa kwa ujumla.

Awali, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Bw. Masha Mshomba, alisema mfuko huo unalenga kuandikisha wananchi waliojiajiri milioni 3.7 ifikapo Juni 2031 kupitia Skimu ya Hifadhi ya Jamii. Alisema takribani asilimia 85 ya nguvu kazi nchini, sawa na wananchi milioni 20.98 wenye uwezo wa kufanya kazi, wamejiajiri, jambo linaloifanya skimu hiyo kuwa nyenzo muhimu ya kuwafikia makundi mbalimbali ya wananchi.

Bw. Mshomba alisema wanachama wa skimu hiyo watanufaika na mafao mbalimbali yakiwemo pensheni ya uzee, mafao ya urithi, ulemavu, uzazi na matibabu. Alisema wananchi sasa wanaweza kujiunga, kuchangia na kufuatilia taarifa zao kwa njia za kidijitali kupitia simu za mkononi, huku kiwango cha chini cha mchango kikiwa shilingi 30,000 kwa mwezi.

Naye, Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF, Bw. Fortunatus Magambo, amesema kiwanda hicho kinazalisha bidhaa zenye ubora wa hali ya juu na kimekuwa na mchango mkubwa kwa jamii na taifa kwa ujumla. 

Alisema kiwanda hicho kimeongeza ajira kwa wananchi, kimeboresha kipato cha wananchi hususan wafugaji kupitia upatikanaji wa soko la uhakika la ngozi, na kuchochea mnyororo wa thamani wa sekta ya mifugo nchini.

“Kiwanda chetu kinazalisha bidhaa zenye ubora mkubwa, kimeongeza ajira kwa wananchi na kimefungua soko la uhakika la ngozi kwa wafugaji wetu, jambo linalonufaisha jamii na taifa kwa ujumla,” alisema Bw. Magambo.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Mahmoud Thabit Kombo (Mb), amewasilisha ujumbe maalum wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Mhe. António Guterres, na kusisitiza dhamira ya Tanzania ya kuimarisha ushirikiano wa kimataifa, amani na maendeleo endelevu.

Baada ya mazungumzo yao, Mhe. Mahmoud Thabit Kombo (Mb) alimkabidhi Mhe. António Guterres zawadi ya kitabu kuhusu Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Rais wa Kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kutambua kuvutiwa kwa muda mrefu kwa Katibu Mkuu huyo na maono, uongozi na mchango wa Mwalimu Nyerere katika kuhimiza amani, maendeleo na ushirikiano wa kimataifa.




Maelfu ya Watanzania wanaofanya kazi katika sekta rasmi na isiyo rasmi wanatarajiwa kupata fursa mpya ya kuweka akiba na kuwekeza kwa muda mrefu kufuatia uzinduzi wa Foresight Private Retirement Fund (FPRF), mfuko mpya wa uwekezaji wa kustaafu uliopata idhini rasmi kutoka Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA).

Mfuko huo unasimamiwa na CORE Securities Limited na unalenga kupanua fursa za uwekezaji na maandalizi ya maisha ya baada ya kustaafu kwa Watanzania wa makundi mbalimbali ya kijamii na kiuchumi.

Uzinduzi na utambulisho rasmi wa mfuko huo umefanyika leo jijini Dar es Salaam, ukihudhuriwa na wadau wa sekta ya fedha, masoko ya mitaji, wawakilishi wa vyama vya wafanyakazi wa sekta ya umma na binafsi, pamoja na wawakilishi wa vyombo vya habari.

Hafla hiyo iliongozwa na Mtaalamu Mbobevu wa Masoko ya Mitaji na Dhamana, Dkt. Ibrahimu Mwangalaba, huku Afisa Mtendaji Mkuu wa CORE Securities Limited, CPA George Fumbuka, akiwaongoza viongozi wengine wa kampuni hiyo kuelezea manufaa na fursa zinazotokana na mfuko huo.

Akizungumza katika hafla hiyo, Dkt. Mwangalaba aliipongeza CORE Securities Limited kwa kuanzisha mfuko huo, akieleza kuwa ni hatua muhimu katika kuimarisha ujumuishaji wa kifedha na kupanua wigo wa huduma za uwekezaji kwa wananchi wengi zaidi.

Alisema kwa muda mrefu mipango ya kustaafu nchini imekuwa ikihusishwa zaidi na watu wenye ajira rasmi ambao ni takribani asilimia chache zaidi ya wananchi wote, hali iliyosababisha sehemu kubwa ya wananchi, hususan walio katika sekta isiyo rasmi, kukosa fursa za maandalizi ya maisha ya baadaye.

“Kupitia FPRF, taifa linapata jukwaa jumuishi linalomwezesha kila Mtanzania — awe ameajiriwa rasmi, amejiajiri, mfanyabiashara au anayejishughulisha na shughuli za sekta isiyo rasmi — kuwekeza na kujiandaa kwa maisha ya baadaye kwa uhuru, unyumbufu na heshima,” alisema Dkt. Mwangalaba.

Aidha, aliwahimiza wananchi kujenga utamaduni wa kuweka akiba na kuwekeza kwa malengo ya muda mrefu, huku akisisitiza umuhimu wa kupata ushauri wa kitaalamu kabla ya kufanya maamuzi ya uwekezaji.

“Mipango ya kustaafu haipaswi kuonekana kama fursa ya watu wachache wenye ajira rasmi pekee. Kila Mtanzania anastahili kuwa na usalama na heshima ya kifedha baada ya miaka yake ya uzalishaji, na mfuko huu ni sehemu ya suluhisho la kufanikisha lengo hilo...nawapongeza sana CORE Securities kwa mpango huu” alisisitiza.

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa CORE Securities Limited, CPA George Fumbuka, alisema FPRF imeundwa kuziba mapengo yaliyopo katika mifumo ya kawaida ya pensheni kwa kutoa chaguzi zenye unyumbufu zaidi katika uwekezaji na upatikanaji wa mafao.

“Ingawa mifuko ya hifadhi ya jamii kama NSSF na PSSSF inaendelea kuwa na mchango mkubwa katika ustawi wa wananchi, FPRF imeundwa kuikamilisha mifumo hiyo kwa kutoa fursa za ziada za uwekezaji kwa watu ambao awali hawakuwa na nafasi ya kushiriki,” alisema.

Alifafanua kuwa CMSA iliidhinisha mfuko huo tarehe 28 Aprili 2026 kwa mujibu wa Sheria ya Masoko ya Mitaji na Dhamana pamoja na Kanuni za Mifuko ya Uwekezaji wa Pamoja za mwaka 1997, huku NMB Bank PLC ikiidhinishwa kuwa Mdhamini na Mlezi wa mfuko huo.

Kwa mujibu wa CPA Fumbuka, mfuko huo umeidhinishwa kukusanya hadi shilingi bilioni 10 kupitia uuzaji wa vipande vya uwekezaji milioni 100, kila kimoja kikiwa na thamani ya shilingi 100.

Alisema muundo wa FPRF umeandaliwa kwa kuzingatia mahitaji tofauti ya kifedha na viwango vya uvumilivu wa hatari za uwekezaji kwa makundi mbalimbali ya umri.

“Mahitaji ya kifedha ya kijana aliyeanza kazi ni tofauti na ya mtu anayekaribia kustaafu. Ndiyo maana tumeandaa mipango tofauti inayowawezesha wawekezaji kuchagua mkakati unaoendana na umri, kipato na matarajio yao ya muda mrefu,” alieleza.

Mfuko huo utakuwa na mipango mitatu ya uwekezaji ambayo ni Youngsters’ Plan kwa wawekezaji wenye umri chini ya miaka 35, Middle-Agers’ Plan kwa wenye umri kati ya miaka 35 na 50, na Seniors’ Plan kwa wawekezaji wenye umri zaidi ya miaka 50, ambao uwekezaji wake utazingatia zaidi dhamana za Serikali.

CPA Fumbuka alibainisha kuwa tofauti na mifuko mingi ya pensheni inayohitaji michango ya muda mrefu kabla ya mafao kupatikana, FPRF ina kipindi cha miaka mitano pekee ambapo baada ya hapo, mwekezaji ataweza kupata fedha zake kwa mkupuo, kwa malipo ya pensheni ya kawaida au kwa mchanganyiko wa njia hizo.

“Mahitaji ya kifedha ya watu hubadilika kadri muda unavyokwenda. Wapo wanaohitaji mapato ya kila mwezi baada ya kustaafu, na wapo wanaoweza kuhitaji sehemu ya akiba zao kwa ajili ya matibabu, familia au biashara. Mfuko huu unawapa uhuru wa kufanya maamuzi hayo kulingana na mahitaji yao,” alisema.

Aliongeza kuwa mwananchi anaweza kuanza uwekezaji kwa kiasi cha shilingi 10,000 tu, sawa na vipande 100 vya uwekezaji, na kuongeza uwekezaji wake taratibu kulingana na uwezo wake wa kifedha.

Mbali na hilo, mfuko huo unatoa faida ya ukwasi (liquidity), ambapo baada ya kipindi cha miaka mitano, wawekezaji wataweza kuuza vipande vyao kwa thamani halisi ya mali za mfuko (NAV), huku malipo yakifanyika ndani ya siku mbili za biashara.

Uwekezaji katika mfuko huo utafanyika kwa njia ya kielektroniki kupitia mfumo wa CORE Securities Limited, matawi maalumu ya NMB Bank PLC pamoja na mawakala walioidhinishwa na kuunganishwa na Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE).

Akizungumza kwa niaba ya Rais wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), Mjumbe wa Kamati ya Utendaji Taifa wa chama hicho, Bw. Nelson Mabula, alisema CWT imejiridhisha kuhusu usalama, uwazi na manufaa ya mfuko huo kwa wanachama wake.

“Kiwango cha chini cha kuanzia uwekezaji cha shilingi 10,000 kinawapa fursa wanachama wetu wengi kushiriki. Tunaamini huu ni uwekezaji wenye manufaa kwa walimu na wafanyakazi wengine, na kama taasisi tutahamasisha wanachama wetu kushiriki ili wawe sehemu ya fursa hii ya kujenga ustawi wao wa kifedha wa muda mrefu,” alisema.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya CORE Securities Limited, CPA George Fumbuka, (kushoto) akimkabidhi Mjumbe wa Kamati ya Utendaji Taifa wa Chama Cha Walimu Tanzania (CWT) Bw. Nelson Mabula (kulia) mfuko wenye nyaraka muhimu kuhusu Mfuko Mpya wa Uwekezaji wa kustaafu unaofahamika kama Foresight Private Retirement Fund (FPRF), ikiwa ni ishara ya uzinduzi wa mfuko huo wakati wa hafla ya uzinduzi iliyofanyika jijini Dar es Salaam leo. Anaeshuhudia katikati ni Mtaalamu Mbobevu wa Masoko ya Mitaji na Dhamana, Dkt. Ibrahimu Mwangalaba. Mfuko huo unasimamiwa na CORE Securities Limited na unalenga kupanua fursa za uwekezaji na maandalizi ya maisha ya baada ya kustaafu kwa Watanzania wa makundi mbalimbali ya kijamii na kiuchumi.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya CORE Securities Limited, CPA George Fumbuka, (kushoto) akimkabidhi Mtaalamu Mbobevu wa Masoko ya Mitaji na Dhamana, Dkt. Ibrahimu Mwangalaba (kulia) mfuko wenye nyaraka muhimu kuhusu Mfuko Mpya wa Uwekezaji wa kustaafu unaofahamika kama Foresight Private Retirement Fund (FPRF), ikiwa ni ishara ya uzinduzi wa mfuko huo wakati wa hafla ya uzinduzi iliyofanyika jijini Dar es Salaam leo. Mfuko huo unasimamiwa na CORE Securities Limited na unalenga kupanua fursa za uwekezaji na maandalizi ya maisha ya baada ya kustaafu kwa Watanzania wa makundi mbalimbali ya kijamii na kiuchumi.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya CORE Securities Limited, CPA George Fumbuka, (kulia) akimkabidhi Mwakilishi kutoka benki ya NMB Bw Avith Massawe (kushoto) mfuko wenye nyaraka muhimu kuhusu Mfuko Mpya wa Uwekezaji wa kustaafu unaofahamika kama Foresight Private Retirement Fund (FPRF), ikiwa ni ishara ya uzinduzi wa mfuko huo wakati wa hafla ya uzinduzi iliyofanyika jijini Dar es Salaam leo. Mfuko huo unasimamiwa na CORE Securities Limited na unalenga kupanua fursa za uwekezaji na maandalizi ya maisha ya baada ya kustaafu kwa Watanzania wa makundi mbalimbali ya kijamii na kiuchumi huku benki ya NMB ikiwa Mdhamini na Mlezi wa mfuko huo.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya CORE Securities Limited, CPA George Fumbuka, (wa pili kushoto) sambamba na Mtaalamu Mbobevu wa Masoko ya Mitaji na Dhamana, Dkt. Ibrahimu Mwangalaba (wa pili kuli), Mjumbe wa Kamati ya Utendaji Taifa wa Chama Cha Walimu Tanzania (CWT) Bw. Nelson Mabula (kulia) na Mwakilishi kutoka benki ya NMB Bw Avith Massawe (kushoto)  wakionesha nyaraka ya muongozo kuhusu Mfuko Mpya wa Uwekezaji wa kustaafu unaofahamika kama Foresight Private Retirement Fund (FPRF), ikiwa ni ishara ya uzinduzi wa mfuko huo wakati wa hafla ya uzinduzi iliyofanyika jijini Dar es Salaam leo. Mfuko huo unasimamiwa na CORE Securities Limited na unalenga kupanua fursa za uwekezaji na maandalizi ya maisha ya baada ya kustaafu kwa Watanzania wa makundi mbalimbali ya kijamii na kiuchumi huku benki ya NMB ikiwa Mdhamini na Mlezi wa mfuko huo.

Akizungumza katika hafla hiyo, Dkt. Mwangalaba  (pichani) aliipongeza CORE Securities Limited kwa kuanzisha mfuko huo, akieleza kuwa ni hatua muhimu katika kuimarisha ujumuishaji wa kifedha na kupanua wigo wa huduma za uwekezaji kwa wananchi wengi zaidi.

Kwa mujibu wa  Mtendaji Mkuu wa CORE Securities Limited, CPA George Fumbuka (pichani) alisema FPRF imeundwa kuziba mapengo yaliyopo katika mifumo ya kawaida ya pensheni kwa kutoa chaguzi zenye unyumbufu zaidi katika uwekezaji na upatikanaji wa mafao.

Meneja wa Mfuko Mpya wa Uwekezaji wa kustaafu unaofahamika kama Foresight Private Retirement Fund (FPRF), Bw Richard Matekele (pichani) akifafanua kuhusu uendeshwaji wa mfuko huo wakati wa hafla hiyo.

Msimamizi wa Mfumo wa Teknolojia wa Mfuko Mpya wa Uwekezaji wa kustaafu unaofahamika kama Foresight Private Retirement Fund (FPRF), Bw Ibrahim Isack (pichani) akifafanua kuhusu uendeshwaji wa mfumo wa teknolojia wa mfuko huo wakati wa hafla hiyo.


Uzinduzi na utambulisho rasmi wa mfuko huo umefanyika leo jijini Dar es Salaam, ukihudhuriwa na wadau wa sekta ya fedha, masoko ya mitaji, wawakilishi wa vyama vya wafanyakazi wa sekta ya umma na binafsi, pamoja na wawakilishi wa vyombo vya habari. 



Top News