Mbunge wa Jimbo la Kibamba, Mhe. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki, amemkabidhi kompyuta Afisa Mteule Daraja la Pili Nassoro Kapiga, Kaimu Mshauri wa Jeshi la Akiba Wilaya ya Ubungo. Makabidhiano hayo yamefanyika katika Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Kibamba, Luguruni, ambapo Mhe. Kairuki amekabidhi kompyuta hiyo kwa lengo la kusaidia kurahisisha utekelezaji wa majukumu ya Afisa Mteule Daraja la Pili Nassoro Kapiga.

Kompyuta hiyo inatarajiwa kuwa nyenzo muhimu katika shughuli za kiutendaji, ikiwemo utunzaji wa taarifa, maandalizi ya nyaraka na matumizi ya teknolojia katika kutekeleza majukumu yake kama Kaimu Mshauri wa Jeshi la Akiba Wilaya ya Ubungo.

Makabidhiano hayo yanaelezwa kuwa sehemu ya kuunga mkono matumizi ya teknolojia katika kuboresha utendaji kazi na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu.Kwa upande wake, Afisa Mteule Daraja la Pili Nassoro Kapiga amemshukuru Mheshimiwa Kairuki kwa msaada Huo.




Na Janeth Raphael MichuziTv 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, (Kazi, Ajira na Mahusiano), Mhe. Deus Clement Sangu (Mb.), amewataka viongozi na wanachama wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa Tanzania (TALGWU) kuhakikisha Uchaguzi Mkuu wa Chama hicho unaendeshwa kwa kuzingatia Katiba, misingi ya demokrasia, uwazi, haki, usawa na amani.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Uchaguzi wa TALGWU uliofanyika Jijini Dodoma, tarehe 17 Septemba 2026, Sangu amesema uchaguzi huo ni sehemu muhimu ya uhai wa Chama na unawapa wanachama fursa ya kuchagua viongozi watakaowaongoza katika kutekeleza majukumu na malengo ya TALGWU.

Sangu amewataka wajumbe kushiriki mchakato wa uchaguzi kwa utulivu na kuheshimiana, akisisitiza kuwa uchaguzi haupaswi kuwa chanzo cha mgawanyiko, bali utumike kama fursa ya kuimarisha umoja na mshikamano wa wanachama. Alieleza kuwa baada ya matokeo kutangazwa, viongozi na wanachama wote wanapaswa kuendelea kushirikiana, kwa kutambua kuwa maslahi ya wafanyakazi ndiyo yanayopaswa kuwa ajenda ya pamoja.

Aidha, Waziri Sangu amesisitiza kuwa Serikali inatambua na kuheshimu uhuru wa vyama vya wafanyakazi, huku akieleza kuwa uhuru huo unaenda sambamba na wajibu wa kuzingatia sheria, Katiba za vyama, uwazi, utawala bora, nidhamu na uwajibikaji. Alisema Serikali inatarajia TALGWU kuendelea kuwa mfano katika uendeshaji wa shughuli zake kwa kuzingatia misingi hiyo.

Waziri huyo pia ameeleza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita itaendelea kushirikiana na TALGWU pamoja na vyama vingine vya wafanyakazi kupitia Mfumo wa Majadiliano ya Pamoja (Social Dialogue), ambapo kero, ushauri na mapendekezo ya wafanyakazi yataendelea kupokelewa na kujadiliwa kwa lengo la kuboresha mazingira ya kazi na maslahi ya wafanyakazi kwa mujibu wa sheria. Aliongeza kuwa changamoto za wafanyakazi zinapaswa kutatuliwa kupitia majadiliano, mashauriano na taratibu zilizowekwa kisheria.

Kwa upande mwingine, Sangu aliwataka viongozi watakaochaguliwa kuzingatia uadilifu, uwazi, uwajibikaji na maslahi ya wanachama katika kutekeleza majukumu yao, huku akiwahimiza wanachama kuendelea kutekeleza wajibu wao kwa weledi, nidhamu na uzalendo. Pia aliwapongeza viongozi na wanachama wa TALGWU kwa mchango wao katika kuimarisha umoja wa wafanyakazi, kutatua changamoto na kuchangia maendeleo ya Chama.







Na Janeth Raphael - MichuziTv

Chama cha Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa Tanzania (TALGWU) kimeiomba Serikali kuchukua hatua za haraka kushughulikia changamoto mbalimbali zinazowakabili watumishi wa umma, kikisema utatuzi wa masuala hayo ni muhimu katika kuboresha mazingira ya kazi, maslahi ya wafanyakazi na utoaji wa huduma kwa wananchi.

Ombi hilo limetolewa leo Septemba 17, 2026 jijini Dodoma na Kaimu Katibu Mkuu wa TALGWU, Wandiba Ngocho, wakati akizungumza katika Mkutano Mkuu wa Taifa wa chama hicho uliohusisha viongozi wa Serikali pamoja na wajumbe kutoka vyama vya wafanyakazi ndani na nje ya Tanzania. Ngocho amesema miongoni mwa changamoto hizo ni ucheleweshaji wa malipo ya fedha za likizo, ambapo baadhi ya watumishi hupokea stahiki hizo kwa awamu au baada ya muda uliopangwa.

Amesema changamoto nyingine ni ucheleweshaji wa malipo ya posho pamoja na leseni za huduma kwa watumishi wa kada za afya, hali ambayo imekuwa ikiwafanya baadhi ya watumishi kusubiri muda mrefu kabla ya kupata stahiki zao. Pia, TALGWU imeeleza kuwepo kwa ucheleweshaji wa malipo ya stahiki za uhamisho kwa watumishi wanaohamishwa kutoka kituo kimoja cha kazi kwenda kingine.

Kwa upande mwingine, chama hicho kimeomba maboresho katika utekelezaji wa mfumo wa Upimaji Utendaji Kazi (PEPMIS), kikieleza kuwa baadhi ya watumishi wanakabiliwa na changamoto katika matumizi yake. TALGWU pia imeibua suala la miundo ya utumishi na mchakato wa kubadilishiwa kada (re-categorization), ambapo baadhi ya watumishi hukumbana na vikwazo licha ya kuwa na elimu na ujuzi unaohusiana na kada wanazohitaji kuhamia.

Ngocho amesema TALGWU pia imebaini changamoto katika utendaji wa baadhi ya Mabaraza ya Wafanyakazi katika halmashauri na taasisi, hali inayopunguza ufanisi wa ushirikishwaji wa wafanyakazi katika masuala yanayohusu ajira na mazingira yao ya kazi. Chama hicho kimeomba hatua zichukuliwe kuimarisha mabaraza hayo pamoja na kuboresha zaidi mazingira ya kazi na maslahi ya watumishi, hususan wanaofanya kazi katika maeneo ya pembezoni.

Akizungumzia umuhimu wa kushughulikia changamoto hizo, Ngocho amesema utatuzi wake utaongeza morali na ari ya watumishi, hivyo kuchangia ufanisi katika utekelezaji wa majukumu na utoaji wa huduma bora kwa wananchi. Aidha, amezipongeza jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan katika kusikiliza na kushughulikia masuala ya wafanyakazi, huku akisisitiza umuhimu wa kuendelea kuimarisha majadiliano kati ya Serikali na wafanyakazi ili kupata ufumbuzi endelevu wa changamoto zinazojitokeza.








Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) umewahimiza wanafunzi na wahitimu wa Vyuo Vikuu Nchini kuanzisha, kujiunga na kurasimisha vikundi vyao vya ujasiriamali ili kuongeza uwezo wa kunufaika na fursa mbalimbali za kiuchumi, ikiwemo mikopo, zabuni na huduma nyingine zinazolenga kuwawezesha vijana.

Wito huo umetolewa leo, Septemba 17, 2026, jijini Dar es Salaam na Afisa Mtendaji Mkuu wa BRELA, Bw. Godfrey Nyaisa, alipokuwa akitoa wasilisho maalum katika Kongamano la CEO Mindset 2026 lililoandaliwa na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na kufanyika katika Ukumbi wa Confucius Institute wa Chuo hapo.

Kongamano hilo lililenga kuwaandaa wanafunzi na wahitimu wapya kuwa viongozi na wasimamizi wenye uwezo wa kuanzisha na kuendesha taasisi, kampuni na biashara zao kwa ufanisi iliwakutanisha wanafunzi 33 kutoka Ndaki ya Biashara (UDBS), Ndaki ya Elimu (UDSoE), pamoja na Ndaki ya Kilimo na Sayansi ya Chakula (CoAF).

Akizungumza katika kongamano hilo, Bw. Nyaisa alisema urasimishaji wa vikundi ni hatua muhimu kwa vijana wanaotaka kujenga biashara endelevu na kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi badala ya vijana kufanya shughuli zao mmoja mmoja, kuunda na kurasimisha vikundi kunaweza kuwawezesha kuwa na nguvu ya pamoja katika kutafuta mitaji, fursa za biashara pamoja na zabuni mbalimbali zinazotolewa na Serikali.

“Vijana mnapaswa kuanza kufikiria zaidi ya mtu mmoja mmoja. Mkiwa katika vikundi vilivyorasimishwa mnaweza kujenga nguvu ya pamoja na kuwa katika nafasi nzuri zaidi ya kutafuta fursa za kiuchumi, usajili na urasimishaji wa biashara ni hatua muhimu katika safari ya kijana kutoka kuwa na wazo la biashara hadi kuwa mjasiriamali mwenye shughuli inayotambulika” alisema Bw. Nyaisa

Bw. Nyaisa alisema elimu ya urasimishaji inapaswa kuanza mapema, hususan katika vyuo vikuu, ili wanafunzi waelewe taratibu za kuanzisha na kusimamia biashara kabla ya kuhitimu huku akiwasisitiza walimu na wahadhiri wa masomo ya biashara Chuoni hapo, kutenga muda katika ratiba zao kwa ajili ya kuwaunganisha wanafunzi na wataalamu wa BRELA kwa lengo la kuwawezesha wanafunzi kupata elimu kuhusu usajili wa kampuni, majina ya biashara na taratibu nyingine za urasimishaji.

Kwa upande wake, Mkuu wa Shule Kuu ya Biashara ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDBS), Prof. Omari Mbura, alimshukuru Afisa Mtendaji Mkuu wa BRELA kwa kutoa elimu kwa wanafunzi waliashiriki Kongamano la CEO Mindset 2026 akisema mchango huo ni sehemu muhimu ya kuwaongezea maarifa yanayohu uongozi, biashara na mazingira halisi ya utendaji baada ya kumaliza masomo. Aliwasisitiza pia wanafunzi kutumia ipasavyo maarifa waliyoyapata na kuendelea kujifunza zaidi.

Nao, baadhi ya wanafunzi waliohudhuria kongamano hilo, walipongeza hatua ya BRELA kupitia kwa Afisa Mtendaji Mkuu Bw. Godfrey Nyaisa kwa kushuka hadi ngazi ya vyuo vikuu kutoa elimu hiyo, akibainisha kuwa imewafungua macho kuona jinsi gani mifumo ya kidijitali ya usajili inavyoweza kuwasaidia kuanza safari zao za kiuongozi na kibiashara wakiwa bado masomoni kupitia vikundi vyao.

Ushiriki wa BRELA katika kongamano hilo ni muendelezo wa Wakala kuwafikia vijana katika maeneo mbalimbali na kuwapatia elimu kuhusu usajili wa biashara, urasimishaji na Miliki Ubunifu, hatua ambayo inaendana na mwelekeo wa maendeleo wa Taifa unaosisitiza uwezeshaji wa wananchi kushiriki katika uchumi na kujenga mazingira ya ukuaji wa sekta binafsi. Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambayo iliridhiwa na Bunge Juni 2025.










Dar es Salaam, Tanzania: The Tanzania National Commission for UNESCO and UNESCO continue to strengthen their cooperation in advancing shared priorities in education, science, culture, communication and information, and sustainable development.


The photograph was taken during an official engagement at the UNESCO Office, UN House, PSSSF Tower Complex, Dar es Salaam, reflecting the continued collaboration between the two institutions in support of UNESCO’s mandate and Tanzania’s development priorities.

Pictured from left: Prof. Hamisi Masanja Malebo, Executive Secretary, Tanzania National Commission for UNESCO; and Mr Michel Toto, UNESCO Country Representative in Tanzania.



📸 Photo: Tanzania National Commission for UNESCO

#UNESCOTanzania #TanzaniaNationalCommissionforUNESCO #UNESCO #Tanzania #SustainableDevelopment
Na Karama Kenyunko Michuzi tv


RAIS Mstaafu wa Awamu ya Nne, Jakaya Mrisho Kikwete, amewataka wanaume kujenga utamaduni wa kupima afya mara kwa mara ili kubaini mapema magonjwa mbalimbali, ikiwemo saratani ya tezi dume.

Kikwete amesema hayo wakati wa hafla ya kuhamasisha uelewa kuhusu saratani ya tezi dume iliyofanyika katika Hospitali ya Kairuki jijini Dar es Salaam, akieleza kuwa uchunguzi wa afya ni muhimu kwa kuwa baadhi ya magonjwa yanaweza kugundulika kabla hayajaanza kuleta madhara makubwa.

Amesema saratani ya tezi dume inaweza kufuatiliwa kwa vipimo vya afya, ikiwemo kipimo cha PSA, huku akisisitiza kuwa wanaume wanapaswa kusikiliza ushauri wa wataalamu wa afya na kuepuka taarifa zisizo sahihi zinazosambazwa kwenye mitandao ya kijamii.

Kikwete ameeleza kuwa saratani hiyo inapogundulika katika hatua za awali, mgonjwa anaweza kupata matibabu kwa wakati, tofauti na pale ugonjwa unapochelewa kugundulika na kusambaa katika maeneo mengine ya mwili.

Amesisitiza pia umuhimu wa wanaume kuwashirikisha wake zao katika masuala ya afya na kufanya maamuzi ya matibabu kwa kuzingatia ushauri wa wataalamu.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Hospitali ya Kairuki, Dkt. Asser Mchomvu alisema asilimia 43.6 ya wagonjwa wa saratani ya tezi dume hufika wakiwa na Ugonjwa uliosambaa.

"Tumedhamiria kuboresha matibabu ya tezi dume hapa nchini hata tukadhubutu kuleta technojia hii mpya na ya Kisasa kuondoa uvimbe bila mwilini bila kufanya upasuaji yaan HIFU,"alisema.

Aidha Mwenyekiti wa Shirika la Afya na Elimu hospitalini hapo, Kokushubila Kairuki alisema katika maadhimisho hayo yaliyoanza Septemba 13, 2026 wanaume 250 walijitokeza kupata ushauri na kupima saratani ya tezi dume

"Mahudhurio yapo chini ukilinganisha na ukubwa wa tatizo, juhudi kubwa zinahitajika kuhamasisha wanaume kupima saratani ya tezi dume mara kwa mara," alisema.





Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Ndugu Abdi Mahamoud Abdi, ameendelea na ziara katika Jimbo la Tumbatu kwa lengo la kukagua uhai wa Chama, kusikiliza changamoto za wanachama na wananchi, pamoja na kuimarisha umoja na mshikamano ndani ya Chama.

Katika ziara hiyo, Ndugu Abdi ametembelea Matawi ya CCM ya Mkokotoni, Mto wa Pwani, Kiongele na Pale, ambako amezungumza na wanachama na wananchi kuhusu changamoto mbalimbali zinazowakabili katika maeneo yao.

Ndugu Abdi amewataka viongozi na wanachama wa CCM kuendelea kudumisha umoja na mshikamano, huku akisisitiza umuhimu wa wanachama kutimiza wajibu wao wa kulipa ada za Chama ili kuwezesha shughuli za CCM kutekelezwa kwa ufanisi kuanzia ngazi ya tawi hadi jimbo.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Wazazi CCM Zanzibar, Ndugu Ali Issa Ali, amesema ziara hiyo ni sehemu ya juhudi za kuimarisha umoja na mshikamano baina ya viongozi na wanachama kuanzia ngazi ya tawi hadi jimbo.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Ndugu Khadija Salum Ali, amesema Wizara inaendelea kuchukua hatua na kuweka mipango ya kuhakikisha changamoto zinazokabili sekta ya elimu katika maeneo ya Kiongele na maeneo mengine zinapatiwa ufumbuzi.

Aidha, Ndugu Abdi ametumia ziara hiyo kuwatembelea na kuwajulia hali baadhi ya Wazee wa Chama, hatua aliyoieleza kuwa ni sehemu ya kuendelea kujenga mshikamano, upendo na utamaduni wa kujali hali za wanachama na viongozi wa CCM.














Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Albert Chalamila amekutana na wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari nchini ikiwa ni mkakati wa Mkoa huo kuimarisha uelewa kwa wananchi kuhusiana na usafi jijini humo, tahadhari ya mvua za Elnino, upangaji wa wafanyabiashara wadogo pamoja na maandalizi ya kupokea wanafunzi wa kidato cha kwanza mwaka 2018 

Akizungumza leo Septemba 17, 2026 jijini Dar es Salaam na wahariri wa vyombo vya Habari RC Chalamila amesema moja ya mambo ambayo Mkoa huo umekusudia kuyafanya ili kuimarisha usafi ni pamoja na kubadili mitazamo ya wananchi ili wawe na utamaduni wa kupenda kufanya usafi na kutenganisha taka kwa kutumia wataalamu kuelimisha jamii pamoja na kusimamia sheria za usafi ipasavyo

Chalamila amesema kuwa katika mkakati huo pia wametoa muda wa miezi mitatu kwa wakandarasi wa uzoaji taka kuwa na vifaa vya kisasa na teknolojia inayoendana na uhitaji wa Mkoa huo, sanjari na kuwezesha usafi kufanyika nyakati za usiku na kuwa na mifumo bora ya uondoshaji maji taka ambapo pia amezungumzia mpango wa kutumia taasisi binafsi kufanya uchakataji taka kupata mbolea na bidhaa zingine.

Akizungumzia suala la wafanyabiashara wadogo RC Chalamila amesema Mkoa huo imeweka mikakati bora ya kuhakikisha biashara ikiwemo za mama lishe zinafanyika kwenye maeneo rasmi na kuondoka maeneo yasio rasmi huku akielekeza TANROAD kuimarisha upandaji miti na utunzaji bustani za barabarani na ametoa muda wa wiki mbili kwa barabara ya uwanja wa ndege (Nyerere Road)

Aidha Mkuu wa Mkoa amezungumzia tahadhari ya uwepo wa Mvua za Elnino kama zilivyotabiriwa na mamlaka ya Hali ya Hewa Nchini TMA na kusema kuwa ni muhimu kwa wananchi kuendelea kuchukua tahadhari kwa kutoziba mitaro, kuepuka utupaji taka hovyo, kusafisha mito sanjari na kuhifadhi chakula huku akisisitiza kuwa s Mkoa huo unaendelea kuboresha miundombinu

Vilevile Chalamila ameeleza mikakati ya Mkoa huo kwa kushirikiana na wadau wa Sekta binafsi kukabiliana na uwepo wa idadi kubwa ya wanafunzi wa kidato cha kwanza mwaka 2018 kutokana na mabadiliko ya mitaala ambapo mwaka 2017 darasa la sita na la saba watahitimu hivyo mbali na ujenzi wa madarasa unaoendelea pia madarasa ya shule binafsi yatatumika

Kwa upande wa Mwenyekiti wa jukwaa la wahariri Tanzania TEF Deudatus Balile amezungumzia taarifa za kidunia zinazoashiria uwepo wa majanga ya mvua kubwa huku akisisitiza usimamizi wa sheria kwenye kuimarisha usafi wa mazingira.













Na Mwandishi Wetu

‎RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, amepongezwa kwa kuwezesha Idara ya Uhamiaji kuendelea kuboresha na kuimarisha matumizi ya teknolojia za kisasa katika utoaji wa huduma za Uhamiaji, hatua inayolenga kurahisisha na kuongeza ufanisi katika taratibu za kuingia na kutoka nchini kwa raia na wageni.

Pongezi hizo zimetolewa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Patrobas Katambi na Kamishna Jenerali wa Uhamiaji CGI Dkt. Anna Makakala wakati wa uzinduzi wa darasa la mafunzo ya mfumo huo katika Chuo Cha Uhamiaji Cha Kikanda TRITA Moshi Mkoani Kilimanjaro Septemba 2026.

‎‎Katika hatua hiyo ya mageuzi ya kidigitali, Idara ya Uhamiaji inatarajia kuanza kutumia mifumo mipya ya kiteknolojia katika vituo vya kuingia na kutoka nchini, ikiwemo Mfumo wa Advanced Passenger Information System (APIS) na Passenger Name Record (PNR).

‎Pia mifumo hiyo itawezesha upatikanaji na uchakataji wa taarifa za abiria kwa njia ya kidigitali kabla na wakati wa safari, jambo litakalosaidia maofisa uhamiaji kupata taarifa muhimu kwa wakati na hivyo kuwezesha huduma za uingiaji na utokaji nchini kutolewa kwa uharaka na ufanisi zaidi.

‎‎Aidha hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuendelea kuwekeza katika teknolojia na mifumo ya kisasa inayolenga kuboresha huduma kwa wananchi na wageni, huku ikiimarisha taratibu za usimamizi wa mipaka na usalama wa Taifa.

‎Kupitia maboresho hayo, Idara ya Uhamiaji Tanzania inaendelea kujikita katika matumizi ya teknolojia ya kidigitali ili kutoa huduma bora, salama, zenye ufanisi na zinazokwenda sambamba na viwango vya kimataifa.

‎Mifumo hiyo mipya inatarajiwa kuanza kufanya kazi hivi karibuni katika vituo husika vya kuingia na kutoka nchini.



Na Abdallah Nassoro - MOI
TAASISI ya Tiba ya Mifupa na Ubongo Muhimbili (MOI) imeanza kutumia technolojia ya kisasa kutoa matibabu ya kibingwa ya upasuaji wa ubongo kwa wagonjwa wa kiharusi inayongeza ufanisi wa matibabu Kwa wagonjwa.

Mkurugenzi wa Upasuaji wa Ubongo MOI Dkt. Lemeri Mchome amesema leo Septemba 17, 2026 kuwa technolojia hiyo ni ya kwanza kutumika nchini na kwamba inakwenda kuleta mapinduzi katika matibabu ya kiharusi.

"Tunatoboa tundu ndogo kichwani na tunapitisha kifaa maalum chenye kamera, Ile kamera inakwenda kutuonyesha eneo ambalo damu imevilia na kutuwezesha kuitoa bila kuathiri sehemu nyingine" amesema Dkt. Lemeri

"Hii ndiyo teknolojia ya kisasa zaidi duniani na sisi kama taasisi hatuko nyuma, wagonjwa wa kiharusi hawana sababu ya kukimbilia nje ya nchi Kwa matibabu, huduma hiyo inapatikana MOI...kwasasa tunapokea wagonjwa watatu hadi watano Kwa siku, teknolojia hii inakuwa msaada wa matibabu bora" ameongeza

Naye Daktari bingwa wa Upasuaji wa Ubongo MOI, Dkt. John Mtei ambaye ameshiriki katika upasuaji wa kwanza kwa kutumia kifaa hicho amesema technolojia hiyo inaacha alama katika mapinduzi ya tiba ya Kiharusi nchini.

"Ufanisi wa matibabu ndiyo nyenzo muhimu katika matumizi ya technolojia hii, mgonjwa anafanyiwa upasuaji na kuondolewa tatizo lake kwa uhakika" amesema Dkt. Mtei

Taasisi ya MOI imeendelea kujikita katika kuleta afua mbalimbali hapa nchini za kuipunguzia Serikali mzigo wa kupeleka wagonjwa nje ya nchi kwa rufaa za gharama kubwa na pia kuendelea kuwa kituo cha weledi cha matibabu ya Mifupa na mfumo wa fahamu barani Afrika





Top News