Bodi ya Maji Bonde la Wami/Ruvu imekutanisha Kikosi Kazi cha Mkoa wa Dar es Salaam na wadau wasafisha mito jijini Dar es Salaam kujadili changamoto zinazoathiri usafi wa vyanzo vya maji na kuweka mikakati ya pamoja ya kukabiliana na athari zinazoweza kujitokeza kutokana na mvua za El Nino zinazotarajiwa kuanza mwezi Oktoba mwaka huu.

Mkurugenzi wa Bodi hiyo, Mhandisi Elibariki Mmassy akizungumza jijini Dar es Salaam, amesema usafi wa mito ni nguzo muhimu katika kulinda vyanzo vya maji, hivyo ushirikiano wa serikali, sekta binafsi na wananchi unahitajika ili kuzuia kuziba kwa njia za maji, mafuriko na uharibifu wa mazingira wakati wa msimu wa mvua.

Kwa upande wake, Katibu Tawala Msaidizi anayesimamia Miundombinu Mkoa wa Dar es Salaam, Mhandisi Amani Mafuru, amesisitiza taasisi na wadau wote kutekeleza wajibu wao kwa wakati ili kuhakikisha mifereji na mito inaendelea kuwa safi, hatua itakayosaidia kupunguza athari zinazoweza kusababishwa na mvua kubwa.

Naye Katibu wa CHAWAMADA, Athumani Kambi, amesema wadau wa usafi wa mazingira wako tayari kushirikiana na mamlaka husika katika kuimarisha shughuli za usafi wa mito, huku akieleza kuwa elimu kwa jamii ni muhimu ili kuondoa tabia ya kutupa taka kwenye vyanzo vya maji.

Mkandarasi Shani Ngwanda amesema utekelezaji wa kazi za usafishaji wa mito utaendelea kuzingatia viwango vya kitaalamu, huku akibainisha kuwa ushirikiano wa wadau wote utasaidia kuongeza ufanisi wa hatua zinazochukuliwa kuimarisha usalama wa mazingira na miundombinu wakati wa msimu wa mvua za El Nino.











Na Mwandishi wetu, Nzega

MWENGE wa uhuru unatarajiwa kuzindua, kukagua, kutembelea na kuweka jiwe la msingi, kwenye miradi ya thamani ya shilingi bilioni 4.1 Wilayani Nzega Mkoani Tabora.

Mkuu wa Wilaya ya Nzega Naitapwaki Tukai ameeleza hayo wakati akikabidhiwa mwenge wa uhuru na Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Uyui Pendo Wella ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Tabora.

DC Tukai amesema ukiwa Wilayani Nzega, mwenge wa uhuru utakimbizwa umbali wa kilometa 223 na kupitia miradi ya thamani ya shilingi bilioni 4.1 ambapo Nzega DC thamani yake ni shilingi bilioni 1.2 na Nzega mji shilingi bilioni 2.9.

Amewapongeza na kuwashukuru wananchi wa maeneo ambayo yamepitiwa na mwenge kwani wamekuwa na hamasa kubwa na mwamko pindi ukipita na kujitokeza kwa wingi kwenye mkesha kata ya Nata.

"Tangu niteuliwe na Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kuwa DC Nzega miaka minne iliyopita sijawahi kuwaona pamoja wabunge wa majimbo ya Nzega vijijini na Bukene wakiwa pamoja ila leo nimewaona na nimefurahi mno," amesema DC Tukai.

Kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru kitaifa mwaka 2026 Wazo Michael Mwangonda amempongeza DC wa Nzega Naitapwaki Tukai kwa namna alivyosimamia maendeleo ya eneo hilo.

"Leo tumeingia Nzega DC kutoka Uyui na tangu tulivyoanza mradi wa kwanza hadi wa mwisho yote ni mizuri na kesho Nzega mji nasikia mambo ni mazuri huko hongera sana Mkuu wetu wa Wilaya," amesema Mwangonda.

Amewaasa wana Nzega waendelee kumpa ushirikiano wa kutosha mkuu wao wa Wilaya ambaye anamwakilisha Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwenye eneo hilo.

Mkimbiza mwenge wa uhuru kitaifa mwaka 2026 kutoka mkoa wa Manyara, Inyasi Amsi amempongeza DC Naitapwaki Tukai kwa namna anavyosimamia maendeleo na ushirikiano kwa wana Nzega.

"Hakika Mheshimiwa DC unatuheshimisha wana Manyara kwani watu wa hapa Nzega wanakupenda kutokana na namna unavyowaongoza na kuwasimamia," amesema Inyasi.


Na Janeth Raphael -MichuziTv

Bodi ya Wataalamu wa Ununuzi na Ugavi (PSPTB) imetangaza matokeo ya Mitihani ya Kati Awamu ya Pili ya Taaluma ya Ununuzi na Ugavi iliyofanyika nchini kuanzia Agosti 30 hadi Septemba 4, 2026, huku watahiniwa 275 kati ya 528 waliofanya mitihani hiyo wakifaulu.

Akizungumza leo, Septemba 18, 2026, jijini Dodoma katika mkutano na waandishi wa habari, Mkurugenzi Mtendaji wa PSPTB, Godfred Mbanyi, amesema mitihani hiyo imeendeshwa kwa mujibu wa Sheria ya Bunge Na. 23 ya mwaka 2007 iliyoanzisha Bodi hiyo, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa majukumu yake ya kuendesha mafunzo na mitihani ya kitaaluma katika fani ya Ununuzi na Ugavi.

Amesema jumla ya watahiniwa 567 walidahiliwa kufanya mitihani hiyo, ambapo watahiniwa 528 sawa na asilimia 93.1 walifanya mitihani, huku 39 wakikosa kwa sababu mbalimbali.

Mbanyi amesema kati ya watahiniwa 528 waliofanya mitihani, 275 sawa na asilimia 52.1 wamefaulu, watahiniwa 232 sawa na asilimia 43.9 wamepewa nafasi ya kurudia masomo yao, huku 21 sawa na asilimia 4.1 wakifeli na kutakiwa kuanza upya masomo katika ngazi husika.

Mbanyi ametoa pongezi kwa watahiniwa waliofaulu katika ngazi mbalimbali, wakiwemo waliokidhi vigezo vya kutunukiwa vyeti vya Professional Diploma, Graduate Professional na CPSP, huku akiwapongeza pia wahadhiri na wakufunzi kutoka vyuo na vituo vya mafunzo kwa mchango wao katika kuwaandaa watahiniwa.

Aidha, amesema PSPTB inawaalika watahiniwa waliokamilisha sifa za Professional Diploma I na II, Graduate Professional I, II na III pamoja na Research kushiriki katika Mahafali ya 15 ya Bodi yatakayofanyika kwa ajili ya kutunuku sifa hizo.

Katika hatua nyingine, Mbanyi amewataka watahiniwa ambao hawakufaulu kujisajili na kurudia masomo yao katika Mitihani ya Kati itakayofanyika kuanzia Novemba 9 hadi 13, 2026. Amesema dirisha la usajili limefunguliwa tangu Septemba 8 na litafungwa Oktoba 24, 2026, huku watahiniwa wenye referral status ya nafasi ya mwisho wakitakiwa kutumia mitihani ya Novemba vizuri, kwani baada ya muda huo hadhi hiyo itaondolewa kwa mujibu wa mtaala wa Bodi.

PSPTB pia imewahimiza wanafunzi waliomaliza vyuo vikuu ndani na nje ya Tanzania kujisajili kwa ajili ya mitihani ya kitaaluma ya Bodi ili kupata sifa stahiki katika fani ya Ununuzi na Ugavi. Wazazi, wadhamini na waajiri nao wametakiwa kuwaunga mkono watahiniwa kwa kugharamia ada za maandalizi na mitihani, hatua ambayo itasaidia kuongeza idadi ya wataalamu wenye maarifa na ujuzi katika sekta hiyo muhimu.



Wilaya ya Ngorongoro ipo katika hatua za mwisho ya mapitio na kupitisha mkakati mpya wa miaka mitano unaodhamiria kufanya mageuzi makubwa ya kiuchumi, kijamii na kasi ya maendeleo unaokwenda sambamba dira ya taifa ya maendeleo 2025-2050.

Akifungua kikao maalum cha kupitia mkakati huo  mkuu wa wilaya ya Ngorongoro Brigedia Jenerali Wilson  Sakulo amewataka madiwani wa halmashauri hiyo kutumia fursa hiyo kwa kupanga vipaumbele vitakavyogusa maisha ya wananchi.

“Leo tumekutana hapa kupanga mipango yetu  kwa miaka mitano, hakikisheni mnapanga  vipaumbele vinavyopimika kwa kuangalia maslahi ya wananchi wa wilaya hii ili waweze kupata huduma bora za kijamii, miundombinu na kuboresha shughuli zao za kiuchumi”,alisema Brigedia Jenerali Sakulo.

Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Ngorongoro Mhe. Manja Sironga Yaile aliipongeza Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kwa kuendelea kuwa mdau muhimu wa maendeleo kutokana na kushiriki kikamilifu katika kuchangia mipango mbalimbali ya kijamii ya Tarafa ya Ngorongoro na wilaya hiyo.

Wakichangia kuhusu mpango mkakati huo baadhi ya madiwani walisisitiza umuhimu wa kujikita katika ujenzi wa barabara,malisho, maji na uimarishwaji wa huduma za kijamii.












Waziri wa Kilimo, Mhe. Daniel Chongolo, ameiagiza Taasisi ya Kuthibiti Ubora wa Mbegu Tanzania (TOSCI) kuhakikisha inaratibu na kusimamia bei za mbegu nchini ili kuwawezesha wakulima kupata taarifa sahihi za bei na kununua mbegu bora kwa bei zinazozingatia taratibu zilizowekwa.

Chongolo ametoa agizo hilo leo jijini Dar es Salaam wakati wa kikao cha wadau wa tasnia ya mbegu akisema mbegu ni miongoni mwa pembejeo muhimu katika uzalishaji wa mazao, hivyo kuna umuhimu wa kuwepo kwa mfumo utakaomwezesha mkulima kufahamu bei ya mbegu kabla ya kufanya manunuzi.

Amesema TOSCI, kwa nafasi yake ya kusimamia ubora wa mbegu nchini, inapaswa pia kuhakikisha kampuni zia mbegu zinasambaza na kuuza mbegu kwa ushindani kwa bei ambazo TOSCI itazisimamia.

“Tumekuwa na utaratibu kwenye mbolea ambapo TFRA ndiyo inayoratibu na kusimamia bei za mbolea”. Mbegu nazo ni pembejeo za kilimo, hivyo hapa TOSCI ina wajibu wa kuratibu,” amesema Mheshimiwa Chongolo.

Aidha, amezitaka kampuni za mbegu kuhakikisha mbegu bora zinawafikia wakulima kwa wakati kupitia mawakala wanaokidhi vigezo, huku akisisitiza umuhimu wa kuongeza uzalishaji wa mbegu nchini. Amesema Tanzania ina ardhi na mazingira bora yanayowezesha kuongeza uzalishaji wa mbegu ndani ya nchi na hivyo kupunguza utegemezi wa mbegu kutoka nje ya nchi.






Na Sixmund Begashe, Dodoma

Timu za Maliasili Sports Club zimetakiwa kucheza kwa nguvu, juhudi na maarifa katika michezo yote ya Michuano ya SHIMIWI 2026, ili kuhakikisha zinaiwezesha Wizara ya Maliasili na Utalii kupata ushindi wa hali ya juu.

Wito huo umetolewa na Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Utawala na Rasilimali Watu wa Wizara hiyo, Bi. Violeth Mlinga, wakati akiiaga timu hiyo kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara, Dkt. Hassan Abbasi, kabla ya kuanza safari kuelekea Moshi, mkoani Kilimanjaro.

Bi. Mlinga amesema Wizara imewaamini wanachama wa klabu hiyo, hivyo amewataka wachezaji kuzingatia weledi, nidhamu na taratibu za Utumishi wa Umma ili kulinda taswira ya Wizara na kuhakikisha timu zinaibuka na matokeo chanya.

Amesema ushiriki wa Wizara katika michuano hiyo ni sehemu ya kuendeleza mahusiano mema ya kiutumishi na Wizara nyingine, sambamba na kutumia michezo kutangaza shughuli na majukumu yanayotekelezwa na Wizara kwa maslahi mapana ya taifa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Maliasili Sports Club, Bw. Elia Mtalemwa, amesema klabu hiyo imejiandaa vyema kwa ajili ya michuano hiyo, huku akieleza kuwa lengo kuu ni kurejea na ushindi katika michezo yote.

Ameushukuru uongozi wa Wizara kwa mchango wake katika maandalizi na ushiriki wa klabu hiyo, akisema timu zote zimejiandaa vyema na zimedhamiria kupambana kwa ajili ya ushindi.

Maliasili Sports Club inaelekea Moshi, mkoani Kilimanjaro, kuungana na timu za Wizara nyingine katika Michuano ya SHIMIWI 2026, itakayowakutanisha watumishi kutoka taasisi mbalimbali za Serikali kushindana katika michezo tofauti.









Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Ndugu Abdi Mahamoud Abdi, amesema CCM imeridhishwa na utekelezaji wa Ilani ya Chama kupitia miradi mbalimbali inayotekelezwa katika sekta ya elimu nchini.

Ndugu Abdi ameyasema hayo wakati akiendelea na ziara ya kukagua uhai wa Chama cha Mapinduzi katika Jimbo la Donge, ambapo alipata fursa ya kukagua ujenzi wa dahalia ya wanafunzi wa kike katika Skuli ya Donge.

Amesema ameridhishwa na maendeleo ya ujenzi wa dahalia hiyo, akieleza kuwa kukamilika kwake kutaimarisha mazingira ya kujifunzia na huduma za elimu kwa wanafunzi wa kike katika eneo hilo.

Aidha, Ndugu Abdi amesema viongozi wakuu wa kitaifa, akiwemo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, wameendelea kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayolenga kuboresha huduma za jamii, kunufaisha wananchi na kukuza uchumi wa nchi.

Amewapongeza Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar (WEMA) kwa usimamizi wa miradi mbalimbali ya elimu, akisema juhudi hizo zitasaidia kupunguza changamoto zinazoikabili sekta hiyo na kuboresha huduma za elimu visiwani Zanzibar.

Kwa upande wao, viongozi wa Jimbo la Donge wamesema eneo hilo limeendelea kupiga hatua za kimaendeleo kutokana na utekelezaji wa miradi mbalimbali katika sekta za kijamii na kiuchumi.

Akitoa taarifa ya kitaalamu, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Ndg. Mwanahamis Adam, amesema kukamilika kwa ujenzi wa dahalia hiyo kutasaidia kuboresha mazingira ya kujifunzia na huduma za elimu kwa wanafunzi wa kike Zanzibar.











Na Marco Maduhu, SHINYANGA


WASTAAFU nchini wametakiwa kuwa makini na watu wanaojitambulisha kama mawakala wa Mfuko wa Pensheni kwa Watumishi wa Umma (PSSSF), wakihimizwa kutumia njia rasmi za mfuko huo katika kuhakiki taarifa zao na kufuatilia mafao yao ili kuepuka kutapeliwa na kupoteza fedha zao.


Tahadhari hiyo imetolewa leo, Septemba 18, 2026, na Afisa Msimamizi wa PSSSF Mkoa wa Simiyu, Salum Mwegelo, wakati wa semina ya PSSSF kwa waandishi wa habari kutoka Klabu za Waandishi wa Habari za Shinyanga na Simiyu pamoja na Mtandao wa Wanablogu Tanzania (Tanzania Bloggers Network – TBN), iliyofanyika mjini Shinyanga.


Mwegelo amesema baadhi ya wastaafu wamekuwa katika hatari ya kutapeliwa kutokana na kutumia watu wasio rasmi wanaodai kuwa wanaweza kuwasaidia katika taratibu za kuhakiki taarifa, kufuatilia au kupata mafao yao.


Amesema watu hao wanaweza kuomba taarifa nyeti za wastaafu, ikiwemo namba za siri za akaunti za fedha na taarifa nyingine binafsi, ambazo zinaweza kutumiwa kufanya miamala bila ridhaa ya wahusika.


“Mawakala hao huwarubuni wastaafu na kuomba namba za siri na taarifa muhimu, ikiwemo taarifa za akaunti zao, na kisha kuzitumia kufanya miamala bila ridhaa ya wahusika na kusababisha kupoteza mafao,” amesema Mwegelo.


Mwegelo amesisitiza kuwa PSSSF haina mawakala wanaotoa huduma kwa niaba ya mfuko huo, hivyo wastaafu wanapaswa kuwa na tahadhari dhidi ya mtu yeyote anayejitambulisha kama wakala wa PSSSF na kuwaomba taarifa zao za siri.


Amesema wastaafu wanapaswa kutumia njia rasmi zinazotolewa na PSSSF, ikiwemo kufika katika ofisi za mfuko huo au kutumia mifumo ya kidijitali inayowawezesha wanachama na wastaafu kufuatilia na kuhakiki taarifa zao kwa usalama.


Amesema matumizi ya mifumo ya kidijitali ni miongoni mwa njia zinazoweza kuwasaidia wanachama kupata taarifa zao kwa urahisi bila kulazimika kuwapa watu wengine taarifa zao binafsi au za kifedha.


Kwa upande wake, Afisa Uhusiano wa PSSSF, Abdul Njalo, amewataka waandishi wa habari na wanablogu kutumia taaluma yao kuwafikishia wananchi taarifa sahihi kuhusu huduma za mfuko huo, hususan elimu inayohusu haki, wajibu na taratibu za kupata mafao.

Njalo amesema vyombo vya habari, blogu na majukwaa ya kidijitali vina nafasi kubwa katika kuhakikisha elimu hiyo inawafikia wanachama na wastaafu kwa lugha rahisi na inayoeleweka, huku akiwataka waandishi na wanablogu kuthibitisha taarifa kabla ya kuzifikisha kwa umma.


Amesema elimu sahihi inaweza kusaidia kuwawezesha wanachama na wastaafu kutambua njia halali za kupata huduma za PSSSF na kuchukua tahadhari dhidi ya watu wanaoweza kutumia mwanya wa ukosefu wa taarifa kuwahadaa.


Naye Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Shinyanga, Greyson Kakuru, amesema semina hiyo imekuwa na umuhimu mkubwa kwa waandishi wa habari na wanablogu kwa kuwa imewapa uelewa zaidi kuhusu huduma za PSSSF na masuala yanayowahusu wanachama na wastaafu.


Kakuru amesema maarifa yaliyopatikana yatawasaidia waandishi na wanablogu kuandaa na kusambaza habari zenye usahihi, huku wakitoa elimu kwa jamii kuhusu namna ya kutumia huduma za PSSSF na kujilinda dhidi ya utapeli.


Amesema ushirikiano kati ya PSSSF na vyombo vya habari pamoja na wanablogu ni muhimu katika kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi kwa wakati na kutumia huduma za hifadhi ya jamii kwa uelewa zaidi.


Naye Mratibu wa Tanzania Bloggers Network (TBN) Kanda ya Ziwa, Kadama Malunde, amepongeza PSSSF kwa kuandaa semina hiyo, akisema mafunzo kama hayo ni muhimu kwa waandishi wa habari na wanablogu kwa kuwa yanawaongezea uelewa wa masuala wanayopaswa kuyafikisha kwa jamii.


Malunde amesema waandishi na wanablogu wana wajibu mkubwa wa kuhakikisha kila taarifa wanayoitoa kwa umma inathibitishwa, ina usahihi na inatoka katika vyanzo vinavyoaminika, hususan katika kipindi hiki ambacho taarifa za kidijitali zinaweza kusambaa kwa kasi kubwa.


“Semina kama hii ni muhimu kwa sababu inatupa nafasi ya kujifunza na kuongeza uelewa. Tukiwa waandishi na wanablogu, jukumu letu si kuchapisha taarifa tu, bali kuhakikisha taarifa tunazowafikishia wananchi ni sahihi, zimehakikiwa na zina manufaa kwa jamii,” amesema Malunde.





Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius Ndejembi, ameuagiza uongozi wa Mkoa wa Dar es Salaam na Halmashauri zake kuhakikisha hali ya Dampo la Pugu inaboreshwa, huku akielekeza maeneo ya makazi yanayozunguka dampo hilo kupuliziwa dawa ili kuwalinda wananchi dhidi ya wadudu na kupunguza hatari ya magonjwa, hususan katika kipindi cha mvua.

Makamu wa Rais ametoa maelekezo hayo leo, Septemba 18, 2026, alipofanya ziara katika Dampo la Pugu linalotumika kukusanya taka za Mkoa wa Dar es Salaam ili kujionea hali halisi ya eneo hilo na kusikiliza kero za wananchi wanaoishi maeneo ya jirani.

Aidha, ameelekeza kuandaliwa kwa mpango kazi wa pamoja utakaoainisha hatua za haraka na za muda mrefu za kukabiliana na changamoto za uendeshaji wa Dampo la Pugu pamoja na kero zinazowakabili wananchi wanaoishi katika maeneo yanayolizunguka, ikiwemo kutopuliziwa dawa za kuua wadudu.

Akiwa katika dampo hilo, Mhe. Ndejembi ameonesha kutoridhishwa na kutofautiana kwa takwimu kuhusu kiasi cha taka zinazokusanywa na kupelekwa katika Dampo la Pugu kila siku kutoka maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Dar es Salaam.

Kutokana na hali hiyo, amezitaka mamlaka zote zinazohusika kukaa pamoja, kuhakiki na kuweka takwimu sahihi zitakazokuwa msingi wa kupanga na kutekeleza hatua madhubuti za kuboresha usimamizi wa taka jijini Dar es Salaam.

“Hatuwezi kutatua changamoto za eneo hili bila kuwa na taarifa na takwimu sahihi. Hawa wananchi mnaowaona wamechoka na stori; wanataka kuona kazi,” alisisitiza Makamu wa Rais.

Makamu wa Rais amesema wananchi wanatarajia kuona matokeo ya moja kwa moja ya hatua zinazochukuliwa na Serikali, hivyo amewataka viongozi na taasisi husika kuharakisha utekelezaji wa maelekezo yaliyotolewa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuhakikisha kero za wananchi zinapatiwa ufumbuzi wa kudumu.

Makamu wa Rais amesema Serikali inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni Serikali sikivu inayojali maslahi ya Watanzania na itahakikisha changamoto za watanzania zinatatuliwa kwa wakati.

Katika hatua nyingine, Mhe. Ndejembi ametoa siku saba kwa mawaziri wanaohusika na TAMISEMI, Maliasili na Utalii pamoja na Ardhi kufika katika maeneo husika na kutatua mgogoro wa muda mrefu unaohusu mipaka ya kiutawala na mpaka wa Msitu wa Kazimzumbwi, ambao umekuwa ukiwaathiri wananchi wa Pugu na maeneo ya jirani.

Changamoto hiyo imesababisha baadhi ya wananchi kutokuwa na uhakika kuhusu maeneo yao ya makazi kutokana na kutofahamika kwa mipaka ya kiutawala pamoja na mpaka wa Msitu wa Kazimzumbwi.

Makamu wa Rais ameelekeza mawaziri hao kufika wenyewe katika maeneo yenye mgogoro na, kwa kushirikiana na wananchi pamoja na wataalamu, kusoma ramani na matangazo rasmi ya Serikali (GN) ili kuweka wazi mipaka na kuwawezesha wananchi kutambua kwa uhakika maeneo yao.

“Waheshimiwa Mawaziri, nataka mfike wenyewe kwenye eneo hili kutambua GN za mikoa na mipaka ya Msitu wa Kazimzumbwi, kwani hii imekuwa kero ya muda mrefu. Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, anataka tutatue kero za wananchi; kwa hiyo naelekeza hili mkalifanyie kazi ndani ya siku saba liwe limeisha,” alisema Mhe. Ndejembi.

Awali, wananchi wa maeneo ya Mstafa, Viwege na Kinyamwezi walitumia fursa ya ziara hiyo kueleza changamoto mbalimbali zinazowakabili, zikiwemo athari zinazotokana na uwepo wa dampo, kutopuliziwa dawa za kuua wadudu katika maeneo yao, ukosefu wa maji kwa muda mrefu pamoja na migogoro ya ardhi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila, ameahidi kusimamia kikamilifu utekelezaji wa maelekezo yote yaliyotolewa na Makamu wa Rais.

Miongoni mwa hatua zitakazotekelezwa ni kuboresha usimamizi wa Dampo la Pugu, kuweka utaratibu wa kila Halmashauri kutenga bajeti mahsusi kwa ajili ya uendeshaji wa dampo hilo, pamoja na kuimarisha upatikanaji wa vifaa na kuboresha miundombinu muhimu ili shughuli za dampo ziendeshwe kwa kuzingatia matakwa ya kimazingira na kiafya.

Hatua hizo zinalenga kuimarisha usimamizi wa taka katika Mkoa wa Dar es Salaam na kuhakikisha changamoto za mazingira, afya na mipaka ya ardhi zinazowakabili wananchi wa Pugu na maeneo ya jirani zinapatiwa ufumbuzi wa haraka na wa kudumu.

Katika ziara hiyo, Makamu wa Rais ameambatana na viongozi mbalimbali wa Serikali, akiwemo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI Mhe. Prof Riziki Shemdoe, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Masauni, Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila, Wakuu wa Wilaya pamoja na viongozi kutoka Halmashauri za Mkoa wa Dar es Salaam.











Top News