
Serikali kupitia Wizara ya Afya imeendelea kuimarisha utayari wa kukabiliana na ugonjwa wa Ebola kwa kuendesha mafunzo kwa vitendo kwa wataalamu wa afya, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuendelea kuimarisha uwezo wa mfumo wa afya katika kuzuia, kugundua na kutoa mwitikio wa haraka dhidi ya magonjwa ya mlipuko.
Hayo yamesemwa Julai 17,2026, na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Dkt. Ibrahim Isack, wakati wa zoezi la usimamizi shirikishi na mafunzo kwa vitendo ya kukabiliana na magonjwa ya mlipuko, amesema kuwa maandalizi ya kutosha ndiyo msingi wa kudhibiti athari za milipuko kwa wananchi.
“Ebola ni ugonjwa unaohitaji umakini mkubwa na hatua za haraka. Wataalamu wa afya wanapaswa kuwa na uwezo wa kutambua viashiria vya awali, kutoa taarifa kwa wakati na kuanzisha hatua za awali za udhibiti ili kuzuia kusambaa kwa maambukizi,” amesema Dkt. Isack.
Amesema usimamizi shirikisishi na mafunzo kwa vitendo hutoa nafasi ya kutathmini utendaji wa huduma za afya katika mazingira yanayofanana na hali halisi, jambo linalosaidia kubaini mapungufu yaliyopo na kuweka mikakati ya kuyafanyia kazi kabla ya kutokea kwa dharura.
Aidha, Dkt. Isack amesema mafanikio katika kukabiliana na magonjwa ya mlipuko yanategemea ushirikiano wa karibu kati ya wataalamu wa afya, viongozi wa sekta ya afya na taasisi mbalimbali, ili kuhakikisha kila ngazi inatimiza wajibu wake kwa wakati na kwa ufanisi.
Kwa upande wake, Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Dharura kutoka wizara ya afya, Dkt. Michael Kiremeji amesema mafunzo hayo yanalenga kuendelea kujenga umahiri wa wataalamu wa afya katika kutoa huduma salama na kufuata taratibu za kitaalamu wakati wa kukabiliana na magonjwa ya mlipuko, hatua inayochangia kuimarisha usalama wa wagonjwa na wahudumu wa afya.
Ameongeza kuwa Wizara ya Afya itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuendesha mafunzo na usimamizi shirikishi katika maeneo mbalimbali nchini, kwa lengo la kuimarisha mfumo wa afya, kuongeza utayari wa kukabiliana na dharura za afya ya umma na kulinda afya za wananchi.
KUTOKA VUNJO
MBUNGE wa Jimbo la Vunjo mkoani Kilimanjaro, Enock amewahimiza vijana kuendelea kumcha Mungu, kuzingatia maadili mema na kujiepusha na vitendo vinavyoweza kuhatarisha maisha na mustakabali wao.
Koola alitoa kauli hiyo leo wakati wa ufunguzi wa bonanza la michezo la vijana wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Jimbo la Kilimanjaro mashariki lililofanyika Marangu mashariki lililowakutanisha vijana 500 kutoka maeneo mbalimbali ya jimbo hilo.
Koola aliwasisitiza vijana kujiepusha na makundi ya kihalifu, kuwa wazalendo na kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo ya jamii na taifa.
Bonanza hilo linalenga kuimarisha umoja, mshikamano na ushirikiano miongoni mwa vijana kupitia ibada, maombi, kujifunza Neno la Mungu na kushiriki michezo mbalimbali inayokuza afya, nidhamu na maendeleo ya kijamii.
Alieleza kuwa, Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Vunjo imeendelea kutekeleza programu mbalimbali zinazolenga kuwawezesha vijana kiuchumi ambapo zinajumuisha mafunzo ya ufugaji wa kuku wa kibiashara, ufugaji wa ng'ombe wa maziwa, ufugaji wa samaki, kilimo cha kisasa na ujasiriamali, kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kujiajiri na kuongeza kipato.
Alisema kuwa, ofisi yake imewaajiri vijana mahsusi ili kuwasaidia wenzao kuunda vikundi vya kiuchumi, kuandaa katiba za vikundi, kukamilisha nyaraka za maombi ya mikopo ya Halmashauri isiyo na riba, pamoja na kuwaunganisha na taasisi za kifedha zinazotoa mikopo yenye masharti nafuu.
Alisisitiza kuwa uwekezaji kwa vijana ni msingi wa maendeleo endelevu ya Jimbo la Vunjo na Taifa kwa ujumla na kuahidi kuendelea kushirikiana na taasisi za dini na wadau mbalimbali katika kuwawezesha vijana kupata elimu, stadi za maisha na fursa za kiuchumi zitakazowasaidia kujenga maisha bora na kuchangia maendeleo ya nchi.
DIWANI wa Kata ya Kinondoni, wilayani Kinondoni, mkoani Dar es Salaam, Idrissa Said Ngatiche (CCM), amesema atafanya jitihada kubwa kuhakikisha watu wenye ulemavu katika kata hiyo wananufaika na kuzifikia fursa muhimu hususan ni za kiuchumi.
Ameyasema hayo leo katika mkutano wa Siku ya Watu Wenye Ulemavu Kinondoni, aliyoandaa maalumu kusikiliza na kutatatua kero za kundi hilo, kula chakulacha pamoja na kukabidhi msaada wa viti mwendo viwili.
Ngatiche amesema, kundi hilo ni muhimu kushirikishwa kikamilifu katika shughuli za kiuchumi ikiwemo kunufaika na mikopo ya asilimia 15 inayotolewa na Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni kwa vikundi vya wajasiriamali wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.
"Kutokana na hali hiyo leo nimeandaa Siku Maalumu ya Watu Wenye Ulemavu Kinondoni, kwa nia ya kuwatambua, kujua idadi yao na kuwasikiliza changamoto zao.Kundi hili limekuwa likisahaulika sana, hivyo kama diwani nimetumia jukwaa hili leo kuwakusanya pamoja ili wanufaike na fursa zilizopo kama makundi mengine,"amesema Ngatiche.
Ameeleza huo ni mwanzo wa hatua zake za kulisaidia kundi hilo huku akitoa wito kwa jamii kuto kuwaficha watu wenye ulemavu hususan watoto ambao wanatakiwa kwenda shule.
"Jamii isiwafiche watu wenye ulemavu. Serikali yetu chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, haijawatenga ndiyo maana katika ile mikopo ya asilimia 15 inayotolewa na halmashauri inatenga asilimia mbili kwaajili ya vikundi vya wenye ulemavu,"ameeleza Ngatiche.
Diwani huyo, amekabidhi viti mwendo viwili kwa watu wenye ulemavu wawili ambao ni mtoto Brighton Michael na mtu mzima Daud Anthon.
Mwenyekiti wa Watu wenye Ulemavu hao Ali Maulid Ali, amempongeza Diwani Ngatiche, kwa jitihada zake za kuwatambua na kuwasaidia watu wenye ulemavu kwani kundi hilo limekuwa likisahaulika.
Maulid amesema kundi kundi hilo linanguvu na halipo kinyonge na mutano huo ni chachu ya kuanzisha umoja wenye nguvu wa watu wenye ulemavu.
" Tunamshukuru sana Rais dk. Samia, nchi iko salama. Yakitokea machafuko sisi wenye ulemavu ndiyo waathirika wakubwa, hivyo tuwakemee watu wanao chochea machafuko. Mkutano huu uwe mwanzo wa sisi watu wenye ulemavu kuwa na umoja wenye nguvu. Hivyo tunamshukuru pia Diwani Ngatiche kwa kuliona hili,"alieleza Maulid.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Ujumbe Maalum kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) Mhe. Félix Antoine Tshisekedi, uliowasilishwa kwake na Waziri wa Ushirikiano wa Kikanda Mhe. Floribert Anzuluni Isiloketshi, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 19 Julai, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Mjumbe Maalum wa Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) Mhe. Félix Antoine Tshisekedi, ambaye ni Waziri wa Ushirikiano wa Kikanda Mhe. Floribert Anzuluni Isiloketshi, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 19 Julai, 2026.

.jpeg)
Na.Mwandishi Wetu
Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela ( NM- AIST) inatumia mbio za marathon kama moja ya mikakati ya kupata fedha za kutoa ufadhili wa masomo kwa wanawake na wasichana ili kuongeza ushiriki wao katika masomo ya Sayansi, Teknolojia, Hisabati na Ubunifu (STEM).
Hayo yamebainishwa Julai 19, 2026 Jijini Arusha wakati wa Maadhimisho ya Mbio za Taasisi hiyo na Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila ambapo amesema kuwawezesha wanawake na wasichana katika masuala ya Sayansi si hisani bali ni uwekezaji wa kimkakati wa Maendeleo ya Taifa
Dkt. Nguvila ameeleza kuwa Dira ya Taifa 2050 inalenga kujenga uchumi wa maarifa unaotegemea ujuzi, utafiti na teknolojia hivyo ametoa wito kwa Taasisi za Elimu ya Juu hususan NM- AIST kuhakikisha tafiti zinazofanyika katika Taasisi hiyoziwe ni zile zizotatua changamoto za wananachi katika sekta za Kilimo, mifugo, madini na viwanda.
Akizungumza awali katika tukio hilo Makamu Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Prof. Maulilio Kipanyula amesema kuwa mbio hizo zilianzishwa mwaka 2024 kuhamasisha wasichana kusoma masomo ya sayansi na kutimiza ndoto zao za kuwa madaktari, wahandisi na watafiti.
"Kwa sasa, Mbio za Mandela zimekuwa alama ya mkoa wa Arusha kwa kuchangia ukuaji wa sekta za michezo, elimu, sayansi, afya na utalii. Tukio hili limeweka msingi imara wa kujenga taifa lenye ujumuishi, mshikamano, na kuandaa kizazi kipya cha wanasayansi na wabunifu wasichana na wanawake," amesema Prof Kipanyula
Mbio hizo zilizohusisha umbali wa kilomita 2.5, 5 10 na 21 zimevuta ushiriki mkubwa wa jamii kutoka ndani na nje ya nchi, na kufanya azma ya kuifanya Arusha kitovu cha sayansi na ubunifu barani Afrika kuwezekana.
Mbio za NM- AIST za Mwaka 2026 zina kauli mbiu isemayo Jitihada kwa Sayansi Hatua kwa Mafanikio.




.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)



.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)







.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
