Na Karama Kenyunko Michuzi Tv

MWANAFUNZI wa Uhandisi Tiba kutoka Chuo Kikuu cha Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) wamekuja na ubunifu wa kifaa kinachoitwa BiliMeasure, kinachotumika kupima kiwango cha bilirubini inayosababisha homa ya manjano kwa watoto wachanga bila kuchukua sampuli ya damu.

Akizungumza katika Maonesho ya Pili ya Ubunifu ya MUHAS (Innovation Week 2026), yaliyofanyika leo Februaria 24, 2026 jijini Dar es Salaam mwanafunzi wa Uhandisi Tiba, Abubakar Mathias, alisema zaidi ya asilimia 60 ya watoto huzaliwa wakiwa na homa ya manjano, hali inayowalazimu kupelekwa kwenye kifaa maalumu cha tiba ya mwanga (phototherapy) kwa matibabu.

Alisema kifaa hicho kitafanya kazi sambamba na phototherapy kwa kupima maendeleo ya matibabu ya mtoto anayeugua manjano. Kifaa hicho huvalishwa mtoto kifuani au kichwani wakati wa matibabu na hupima kiwango cha bilirubini papo kwa papo bila maumivu.

“Kwa sasa vipimo vya manjano hutegemea sampuli ya damu, hali inayosababisha maumivu kwa watoto wachanga na usumbufu kwa wazazi pamoja na watoa huduma. Pia majibu ya maabara huchukua zaidi ya saa 12 hadi 24,” alisema.

Alieleza kuwa kifaa hicho kinatoa majibu ya muda halisi na hutoa taarifa kila baada ya dakika tano, hivyo kuondoa ucheleweshaji wa majibu ya maabara.

Mbali na kuondoa maumivu ya utoaji damu, kifaa hicho pia kinasaidia kudhibiti matumizi ya muda mrefu ya phototherapy (over treatment) ambayo inaweza kuleta madhara ikiwemo athari za mwanga kwa mtoto. Mtoto anapofikia kiwango stahiki cha bilirubini, kifaa hutoa alama ya sauti na mwanga kumuarifu mtoa huduma ili kuzima kifaa cha tiba ya mwanga.

Mathias alisema wamechukua mwaka mmoja kufanya utafiti, kuanzia hatua ya wazo, kufanya tafiti hospitalini na kwa watumishi wa afya, hadi kufikia hatua ya maendeleo ya kifaa hicho. Kwa sasa wanaendelea na maboresho ili kiweze kupitishwa na kutumika rasmi hospitalini, huku kilichobaki zaidi kikiwa ni uboreshaji wa muonekano wa nje (industrial design) na uchaguzi wa vifaa vya nje.
Mwanafunzi wa Uhandisi Tiba kutoka chuo Kikuu cha Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) mwenye fulana ya bluu akifafanua jambo kwa mtazamaji namna kifaa cha kupima homa ya manjano kwa watoto (billimeasure) kinavyofanya kazi wakati wa maonesho ya pili ya ubunifu ya MUHAS (Muhas innovation week 2026) leo Februari 24,2026
MWANAFUNZI wa mwaka wa tatu katika Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (Muhas), Jocelyne Joshua, amesema wao kama kikundi cha Tanzania Biomedical Engineering Students Association (TABESA) wamebuni teknolojia maalum itakayowawezesha watu wenye changamoto ya usikivu kujumuika kikamilifu katika jamii na kueleweka kwa urahisi.

Jocelyne ambaye anasomea ya Shahada ya Uhandisi Tiba amesema awali waliamini kuwa watu wenye changamoto ya usikivu ni lazima wawe na msaidizi wa pembeni kwa ajili ya kutafsiri lugha za alama, lakini uhalisia ni kwamba wasaidizi hao ni wachache sana hali inayowafanya wahusika kukutana na watu wengi wasioweza kuwasiliana nao kwa lugha ya alama.

Amesema bunifu hiyo imekuja na application yenye uwezo wa kubadili alama za vidole na kuzipeleka moja kwa moja katika maneno na sauti ili kusaidia katika mawasiliano.

“Kwa mfano, walimu wanaofundisha watoto wenye changamoto hizi inapaswa wawe wanazijua lugha za alama au wawe na mtu wa pembeni atakayewasaidia kuwaelewesha wanafunzi darasani na kuwasaidia kuelewa masomo,” amesema.

Alisema kwa kutumia teknolojia hiyo, inaweza kuunganishwa darasani ambapo mwalimu akifundisha, mwanafunzi ataweza kuona kwenye screen kile ambacho mwalimu anazungumza hata kama mwalimu hajui lugha ya alama.

Kwa sasa wana bidhaa tatu; ya kwanza ni application inayoitwa Sauti App, ya pili ni tovuti inayoitwa Sauti Web, na pia wanatarajia kuja na kifaa maalum kwa ajili ya wale wanaopata changamoto ya kumudu au kupata simu janja ili kiwasaidie katika mawasiliano wanapokuwa wanatembea.

Amesema tayari wameshafanya usajili BRELA na sehemu nyingine husika ili kadri wanavyoendelea kuboresha bidhaa zao iwe rahisi kuzipeleka sokoni kwa kuwa tayari zimetambulika.

TABESA ni kikundi cha wanafunzi wa mwaka wa tatu wa Biomedical Engineering chenye wanafunzi wa fani mbalimbali, akiwemo mmoja ambaye hasikii wala haongei lakini bado anachangia mawazo yake kikamilifu katika utekelezaji wa mradi huo.

Serikali kupitia Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) imetia saini mkataba wa uwekezaji katika sekta ya madini kwa ajili ya kuendeleza leseni ya uchimbaji wa dhahabu katika eneo la Kigosi, mkoani Geita.

Hatua hiyo inaelezwa kuwa chachu mpya ya kukuza uchumi wa eneo hilo na taifa kwa ujumla.

Hafla ya utiaji saini imefanyika Februari 24, wilayani Bukombe mbele ya Naibu Waziri wa Madini, Steven Kiruswa, aliyekuwa mgeni rasmi.

Mkataba huo umehusisha pande mbili ambazo ni STAMICO na kampuni ya Plantcor Mining and Plant Hire PTY Ltd ya Afrika Kusini, ambayo itawekeza katika uendelezaji wa mradi huo wa dhahabu.

Kiruswa ametoa maagizo kwa STAMICO pamoja na mwekezaji kuhakikisha kuwa uwekezaji huo unatekelezwa kwa vitendo na kuanza kazi mara moja bila kupoteza muda, ili uweze kuleta manufaa kwa wananchi wa Kigosi na maeneo jirani.

Aidha, amesisitiza kuwa mradi huo unapaswa kupanua wigo wa shughuli za uchimbaji katika eneo la Kigosi ili kuwapa nafasi wachimbaji kupata maeneo halali ya kuendelea na shughuli zao.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa STAMICO, Simon Sirro, amewaomba wananchi waliokuwa wakifanya shughuli katika pori la Kigosi kushirikiana na uwekezaji huo mpya na kuepuka kuwa chanzo cha vikwazo, hasa kutokana na mazoea yaliyokuwepo kabla ya mradi kuanza rasmi.

Sambamba na hilo, Naibu Waziri Kiruswa amesisitiza umuhimu wa kampuni mwekezaji kuzingatia masuala ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR), ili kuhakikisha kuwa jamii zinazozunguka eneo la Kigosi na wilaya ya Bukombe zinanufaika moja kwa moja kupitia miradi ya maendeleo kama vile elimu, afya na miundombinu.

Mkataba huo unatarajiwa kuleta manufaa makubwa kwa Watanzania, ikiwa ni pamoja na Kuongeza ajira kwa vijana, Kuongeza mapato ya serikali,Kuchochea ukuaji wa uchumi wa vijiji vinavyozunguka Kigosi pamoja na Kukuza sekta ya madini nchini

Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Venance Mwasse, amesema kuwa mradi huo utaanza kwa kufanya utafiti wa kina wa kijiolojia, uchorongaji na uthibitishaji wa rasilimali.

Aidha, hatua zitakazofuata ni pamoja na upembuzi yakinifu wa kiuchumi, maendeleo ya mgodi, ujenzi wa miundombinu muhimu na usimikaji wa mtambo wa uchenjuaji wa dhahabu.

Uwekezaji huu wa dhahabu katika eneo la Kigosi unaonekana kuwa fursa muhimu kwa maendeleo ya mkoa wa Geita na taifa kwa ujumla. Ushirikiano kati ya serikali, mwekezaji na wananchi utakuwa nguzo kuu ya kuhakikisha mradi huu unaleta matokeo chanya na endelevu kwa kizazi cha sasa na kijacho.










Mbunge wa Jimbo la Itwangi, Mhe. Azza Hilal Hamad akizungumza katika kikao cha Bodi ya Barabara Mkoa wa Shinyanga.

Mbunge wa Jimbo la Itwangi, Mhe. Azza Hilal Hamad akizungumza katika kikao cha Bodi ya Barabara Mkoa wa Shinyanga.

Mbunge wa Jimbo la Itwangi, Mhe. Azza Hilal Hamad akiwa kwenye kikao cha Bodi ya Barabara Mkoa wa Shinyanga.


Na Kadama Malunde – Malunde 1 Blog


Mbunge wa Jimbo la Itwangi, Azza Hilal Hamad, ameomba Serikali kuipandisha hadhi barabara ya Didia–Solwa ili iweze kuhudumiwa kwa kiwango kinachostahili kulingana na umuhimu wake kiuchumi na kijamii.


Maombi hayo ameyatoa Februari 24, 2026 katika kikao cha Bodi ya Barabara Mkoa wa Shinyanga kilichohudhuriwa na viongozi mbalimbali wa mkoa.


Mhe. Azza amesema uboreshaji wa barabara hiyo utarahisisha usafirishaji wa mazao, kuimarisha upatikanaji wa huduma za kijamii na kufungua fursa zaidi za kiuchumi kwa wananchi wa Didia na Solwa. Sambamba na hilo, ameomba kuwekewa lami kipande cha barabara kutoka njiapanda ya Didia (Puni) hadi Didia Senta ili kuboresha miundombinu ya usafiri na kuchochea maendeleo ya biashara katika eneo hilo.


Ameeleza kuwa Didia Senta inatarajiwa kuwa kitovu muhimu cha uchumi kutokana na ujenzi wa Kituo cha Reli ya Kisasa (SGR), hivyo uboreshaji wa barabara hiyo utawezesha mtiririko mzuri wa watu na mizigo na kunufaisha wananchi pamoja na wawekezaji.


Aidha, amesisitiza kuwa barabara ya Didia–Solwa ikipandishwa hadhi, itaanza kusimamiwa na Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS) badala ya Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA), hatua ambayo itaipa uzito wa kitaifa na kuongeza uwezo wa kupata rasilimali za kutosha kwa ajili ya matengenezo na maboresho ya kudumu.


Halikadhalika, Mhe. Azza ameomba pia barabara ya Didia/Kabanga/Mwamalulu kwenda Isakajana katika Jimbo la Msalala ipandishwe hadhi, hatua itakayorahisisha usafiri wa wananchi na kurahisisha usafirishaji wa bidhaa kati ya mikoa na wilaya zinazozunguka eneo hilo.


Katika kuimarisha usalama barabarani, Mbunge huyo pia ameiomba Serikali kuweka taa za barabarani katika njiapanda ya Tinde na Didia pamoja na kufunga taa za kuongozea magari katika njiapanda ya Tinde, kufuatia ongezeko la magari na watembea kwa miguu katika maeneo hayo.

Akizungumza katika kikao hicho, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mboni Mhita, amesisitiza dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita kuendelea kuimarisha miundombinu ya barabara kupitia TANROADS na TARURA, huku akisisitiza usimamizi madhubuti ili kulinda uwekezaji mkubwa unaofanywa katika sekta hiyo.


“Suala la taa ni kipaumbele. Waheshimiwa wabunge wamezungumzia uwepo wa taa katika maeneo mbalimbali, hatua ambayo imechochea ukuaji wa maeneo na mzunguko wa kiuchumi. Tunaangalia namna ya kuongeza taa, mfano pale Tinde, ambayo ni moja ya senta zinazohitaji taa za uhakika,” amesema Mhita.


“Ajenda ya Barabara ya Kolandoto ni kipaumbele cha mkoa wa Shinyanga. Kuhusu barabara ya Didia–Solwa, Mhe. Mbunge Azza Hilal ameomba ipandishwe hadhi. Kwa kuwa Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Shinyanga yupo hapa, anajua hatua za haraka kuchukua ndani ya wiki hii. Andiko la barua litufikie mkoani ili tuweze kusukuma barabara yetu ipandishwe hadhi kutoka TARURA hadi TANROADS, na hatimaye kuipatia fedha za lami”,ameongeza Mhe. Mhita.












Shirika la MyLEGACY limekutana na waandishi wa habari na wadau wa vyombo vya habari katika kikao cha ushirikishwaji chenye lengo la kuimarisha uelewa wa umma kuhusu mabadiliko ya tabianchi na kuiweka sekta ya habari kama jukwaa muhimu la utetezi wa masuala ya mazingira na usawa wa kijinsia.

Kikao hicho ni sehemu ya utekelezaji wa mradi wa Kukuza Hatua za Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi Zinazozingatia Usawa wa Kijinsia kwa Kesho iliyo Bora (Kesho Njema) unaotekelezwa kwa msaada wa Embassy of Ireland in Tanzania.

Akizungumza katika kikao hicho, mwakilishi wa MyLEGACY amesema jamii nchini zinaendelea kukabiliwa na athari za mabadiliko ya tabianchi zikiwemo mafuriko, ongezeko la joto la muda mrefu na uhaba wa maji, hali inayoathiri zaidi wanawake, wasichana na watu wenye ulemavu.

Imeelezwa kuwa mabadiliko ya tabianchi yanaongeza pengo la kijinsia, yanaongeza hatari za ukatili wa kijinsia na kuvuruga upatikanaji wa huduma za afya ya uzazi.

Hata hivyo, mifumo mingi ya mipango ya kukabiliana na tabianchi bado haijaingiza kikamilifu mwelekeo wa kijinsia katika tathmini ya udhaifu na ustahimilivu wa jamii.

Tathmini Yabaini Mapungufu katika Mipango ya Tabianchi

Kupitia mradi wa Kesho Njema, MyLEGACY imefanya tathmini ya mipango ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi katika Wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam, kwa kuangazia jinsi inavyojumuisha haki za afya ya uzazi na hatua za kuzuia ukatili wa kijinsia.

Tathmini hiyo ilichambua mipango ya kuanzia mwaka wa fedha 2013/14 hadi 2024/25 katika ngazi za kata, shule za msingi na sekondari, pamoja na miundo ya utawala wa jamii.

Matokeo ya tathmini yanaonesha kuwa mipango mingi imejikita zaidi katika maboresho ya miundombinu kama usafishaji na urekebishaji wa mifereji ya maji taka pamoja na usafi wa mazingira.

Hata hivyo, masuala ya haki za afya ya uzazi na ukatili wa kijinsia hayajajumuishwa ipasavyo katika mifumo rasmi ya mipango ya tabianchi.

Aidha, imebainika kuwa ushirikiano kati ya idara za mazingira, afya na jinsia bado ni mdogo, takwimu za kijinsia kuhusu athari za tabianchi hazitoshelezi, na ushiriki wa wanawake, vijana na makundi yaliyotengwa katika maamuzi ya tabianchi ni mdogo.

Kutokana na hali hiyo, tathmini imependekeza kuingizwa kwa viashiria vya haki za afya ya uzazi na mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia katika mikakati ya ngazi za mitaa, kuimarisha uratibu wa kisekta, kuweka bajeti za tabianchi zinazozingatia jinsia na kupanua ushiriki wa wanawake na vijana.

Wanafunzi 775 Wawezeshwa Kuwa Mabalozi wa Tabianchi

Mradi huo pia umefikia wanafunzi 775 wenye umri wa miaka 9 hadi 17 kutoka shule 25 kupitia vilabu vya WASH, kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kuelewa na kushiriki katika masuala ya tabianchi.

Kupitia midahalo, igizo, sanaa na kazi za vikundi, wanafunzi waliwezeshwa kuelewa uhusiano kati ya mabadiliko ya tabianchi, usawa wa kijinsia na haki za afya ya uzazi.

Mbinu hizo shirikishi zimeelezwa kuongeza ushiriki na uhifadhi wa maarifa miongoni mwa wanafunzi.

MyLEGACY imesema kuwa kuwawezesha wanafunzi kuwa “Mabingwa wa Nishati” na mawakala wa mabadiliko kunasaidia kujenga uwajibikaji na kuhamasisha mabadiliko chanya shuleni na katika jamii wanazotoka.

“Mgahawa wa Maarifa”

Waibua Sauti za Jamii

Kupitia jukwaa lake la Mgahawa wa Maarifa, MyLEGACY limefanya midahalo ya kijamii iliyowakutanisha washiriki 249 wakiwemo viongozi wa mitaa, wanawake, vijana, walimu na watu wenye ulemavu.

Majadiliano hayo yamebainisha kuwa jamii zina uelewa wa kina kuhusu changamoto za kimazingira na zina uwezo wa kupendekeza suluhisho endapo zitapatiwa jukwaa salama na jumuishi.

Aidha, imeelezwa kuwa mjadala wa tabianchi unapaswa kuzingatia mwingiliano wa masuala ya kijinsia, ulemavu, elimu na afya, huku kukisisitizwa umuhimu wa kuimarisha mifumo ya utekelezaji ili kuziba pengo kati ya maarifa na vitendo.

Miti 2,000 Yapandwa Mashuleni

Katika hatua za utekelezaji wa vitendo, MyLEGACY imewezesha upandaji wa miti 2,000 ya kivuli na matunda katika shule 24 kupitia vilabu vya WASH na Mazingira. Miti hiyo inatarajiwa kuboresha mazingira ya shule kwa kupunguza joto na vumbi pamoja na kuongeza ustawi wa wanafunzi.

Wanafunzi pia walipata mafunzo ya vitendo kuhusu upandaji na utunzaji wa miti, ikiwemo matumizi ya mifumo rahisi ya umwagiliaji kama drip irrigation kwa kutumia chupa za plastiki zilizotumika.

Shirika hilo limesema kuwa ushirikiano kati ya wanafunzi, walimu, uongozi wa shule na wanajamii umeimarisha uwajibikaji wa pamoja katika uhifadhi wa mazingira na kuhakikisha uendelevu wa hatua za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Kwa ujumla, MyLEGACY imesisitiza kuwa mafanikio ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi yanategemea ushirikiano wa sekta zote, hususan vyombo vya habari, katika kuelimisha umma na kusukuma ajenda ya tabianchi inayozingatia usawa wa kijinsia kwa maendeleo endelevu.



NA EMMANUEL MBATILO, MICHUZI TV

Serikali imesema Tanzania inaendelea kupiga hatua kubwa katika ukuaji wa matumizi ya teknolojia, hatua inayochochea maboresho katika sekta mbalimbali ikiwemo utoaji wa huduma za kisheria.

Akifungua mkutano wa siku mbili ulioanza leo Februari 24, 2026 Jijini Dar es Salaam kuhusu Teknolojia na Msaada wa Kisheria uliofanyika katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Zainabu Katimba, alisema kuwa matumizi ya teknolojia si chaguo bali ni hitaji la lazima katika ulimwengu wa sasa.

“Ukuaji wa teknolojia unatoa fursa mpya za kuboresha upatikanaji wa huduma za msaada wa kisheria kwa jamii. Serikali inaangalia kwa makini namna teknolojia itakavyotumika kurahisisha utoaji wa huduma hizo,” alisema Katimba.

Mkutano huo uliwakutanisha wadau wa sheria na teknolojia kutoka nchi wanachama wa Jumuia ya Afrika Mashariki, ukiwa na lengo la kujadili mbinu bunifu za kutumia teknolojia kuongeza ufanisi na upatikanaji wa haki.

Akizungumza mara baada ya ufunguzi wa mkutano huo, Mkuu wa Idara za Sheria za Umma kutoka Shule Kuu ya Sheria, Dkt. Boniphace Luhende, akimwakilisha uongozi wa kitaaluma, alisema kuwa kongamano hilo ni jukwaa muhimu la kujifunza na kubadilishana uzoefu.

“Teknolojia ina uwezo mkubwa wa kurahisisha upatikanaji wa haki, hasa kwa wananchi wa maeneo ya mbali. Mkutano huu utasaidia washiriki kuelewa namna bora ya kuitumia,” alieleza.

Kwa upande wake, Dkt. Cecilia Ngaiza kutoka Shule Kuu ya Sheria ya chuo hicho, alisema kuwa majadiliano hayo yatawawezesha washiriki kushirikishana maarifa na uzoefu katika masuala ya kisheria yanayohusiana na teknolojia.

Naye Mhadhiri wa Shule Kuu ya Sheria, Dkt. Petro Protus, alisema lengo kuu la mkutano huo ni kutafuta suluhisho la jinsi wananchi wanavyoweza kupata huduma za kisheria kwa urahisi kupitia mifumo ya kidijitali.

“Tunajadili njia za kuhakikisha teknolojia inakuwa daraja la haki kwa wananchi wote,” alisema.

Wadau wa mkutano huo walisisitiza kuwa matumizi sahihi ya teknolojia katika sekta ya sheria yanaweza kuongeza uwazi, kupunguza gharama na muda wa mashauri, pamoja na kupanua wigo wa msaada wa kisheria kwa wananchi.

Kwa ujumla, ukuaji wa teknolojia katika sekta ya sheria unatarajiwa kurahisisha upatikanaji wa suluhu na haki kwa wananchi kwa wakati na kwa ufanisi zaidi.








Serikali imesema Mkutano wa Jukwaa la Wakurugenzi wa Bodi na Watendaji Wakuu wa Kampuni ambazo Serikali ina hisa chache (Minority Interests Forum-MIF 2026) utakuwa jukwaa mahususi la kujadili, pamoja na mambo mengine, mikakati ya kuharakisha safari ya Tanzania kuelekea uchumi wa kati wa juu ifikapo mwaka 2050.

Mkutano huo, unaoratibiwa na Ofisi ya Msajili wa Hazina (OMH), utafanyika kuanzia Machi 16 hadi 18, 2026 katika Ukumbi wa PAPU, jijini Arusha, na unatarajiwa kuwakutanisha Wakurugenzi wa Bodi na Watendaji Wakuu kati ya 150 na 200 kutoka kampuni 56 ambazo Serikali inamiliki hisa chache, yaani chini ya asilimia 51.

Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika jijini Dar es Salaam Februari 24, 2026, Mkurugenzi wa Usimamizi wa Utendaji, Ufuatiliaji na Tathmini – Mashirika ya Kibiashara, Bi. Lightness Mauki, alisema kuwa safari ya Tanzania kuelekea uchumi wa kati wa juu si ya kubahatisha, bali ni matokeo ya maamuzi ya kimkakati, usimamizi thabiti na uongozi unaotazama mbele.

“Tunakwenda kujadili namna ya kukabiliana na mabadiliko ya kiuchumi na kiteknolojia ili tuweze kufikia lengo la uchumi wa kati wa juu katika kipindi cha miaka 24 ijayo kama ilivyobainishwa kwenye Dira 2050,” alisema Bi. Mauki.

Alieleza kuwa kaulimbiu ya mwaka huu — ‘Kutoka ufuatiliaji na usimamizi wa kawaida kwenda katika uongozi na usimamizi unaoangalia mbele’ — inalenga kuhamasisha mageuzi ya fikra kutoka ufuatiliaji wa kawaida wa utendaji kwenda katika uongozi bunifu na unaotazama mbele, unaotambua mapema vihatarishi na kutumia fursa za kimkakati katika mazingira ya mabadiliko ya haraka ya kiuchumi na kiteknolojia.

Tanzania imejiwekea lengo la kimkakati la kukuza uchumi wake kutoka takriban dola za Marekani bilioni 85 hadi kufikia dola trilioni 1 ifikapo mwaka 2050 kupitia utekelezaji wa Dira 2050, inayolenga kujenga uchumi wa juu wa kati, wenye ushindani na jumuishi.

Alisisitiza kuwa kufikia lengo hilo kunahitaji kuachana na usimamizi wa kimazoea na kuimarisha ushirikiano kati ya sekta ya umma na sekta binafsi.

“Tunahitaji usimamizi ambao si wa kimazoea na lazima tufanye kazi kwa kushirikiana na sekta binafsi,” alisema.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa kulinda rasilimali na mipaka ya nchi kwa wivu mkubwa ili kuhakikisha uwekezaji unaingiza thamani halisi kwa Taifa.

“Lazima tulinde rasilimali na mipaka ya nchi yetu kwa wivu mkubwa,” aliongeza.

Bi. Mauki alisema OMH itaendelea kuhakikisha uwekezaji wote katika kampuni ambazo Serikali ina hisa chache unakuwa na tija, unaleta matokeo yanayotarajiwa na unaichangia Tanzania kusogea karibu zaidi na lengo la uchumi wa kati wa juu.

Kupitia jukwaa hilo, viongozi wa kampuni watajadili uoanifu wa mikakati ya taasisi zao na Dira 2050, matumizi ya teknolojia katika kuimarisha uwazi na uwajibikaji, pamoja na uchambuzi wa taarifa za kiuchumi na kiushindani katika kuboresha maamuzi ya uwekezaji.

Katika kipindi cha miaka minne iliyopita, kampuni hizo zimeendelea kuonesha mchango mkubwa katika uchumi wa Taifa kwa kuimarisha mapato ya Serikali kupitia kodi na gawio, kuongeza ajira na kuchochea ukuaji wa sekta mbalimbali za kimkakati.

Takwimu rasmi zinaonesha mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kipindi hicho.

Thamani ya uwekezaji wa Serikali katika kampuni hizi imeongezeka kutoka shilingi bilioni 821.51 mwaka 2020 hadi shilingi trilioni 1.94 mwaka 2024, sawa na ongezeko la asilimia 136.

Mapato ghafi yameongezeka kutoka shilingi trilioni 6.81 hadi shilingi trilioni 10.74, sawa na ongezeko la asilimia 58, huku faida ikiongezeka kutoka shilingi trilioni 1.79 hadi shilingi trilioni 1.95.

Katika kipindi cha 2020 hadi 2024, kampuni hizi zimechangia takribani shilingi trilioni 3.67 kama kodi ya mapato ya kampuni.

Aidha, gawio kwa Serikali limeongezeka kutoka shilingi bilioni 58.26 hadi shilingi bilioni 266.52, sawa na ongezeko la asilimia 357.

Kwa mtazamo wa Bi. Mauki, mafanikio hayo yanaonesha kuwa mwelekeo uliopo ni sahihi, lakini bado kuna wajibu wa kuongeza kasi, ubunifu na ufanisi katika uongozi wa kampuni hizo ili kuhakikisha Tanzania inafikia malengo yake ya kiuchumi ifikapo mwaka 2050.

“Tunapoelekea mwaka 2050, tunahitaji uongozi thabiti, unaotazama mbele na unaochukua hatua mapema. Huu si wakati wa kusubiri matokeo; ni wakati wa kuyatengeneza,” alihitimisha.




Na Diana Byera, Bukoba

WADAU wa brabara mkoani Kagera wamepata fursa ya kupokea taarifa  za mapendekezo ya bajeti kutoka kwa  Wakala wa Barabara Tanzania (TANROAD) pamoja na Wakala  wa Barabara za Mjini na Vijijini(TARURA).

Akizungumza mbele ya wadau hao Meneja wa TANROAD Mkoa wa Kagera Joel Samwel amesema TANROAD  wanakadiria kutumia Sh.bilioni 14.5 kwa mwaka wa fedha 2026/2027  kwa ajili ya  matengenezo ya barabara na madaraja.

Ameongeza kuwa ingawa bajeti halisi ya kusaidia matengenezo ya barabara madaraja  inayoweza kutosheleza vizuri Barabara za mkoa wa Kagera ni Sh.bilioni 25.8

Amesema Serikali imeendelea kutoa fedha za kukamilisha madaraja matano ya dharura ambayo yaliathiriwa na mvua kubwa za Elnino na sasa wananchi wataanza kutumia sehemu ya hizo kwa kipindi Cha mwaka mzima

Kwa upande wake Kaimu Meneja wa TARURA Mkoa wa Kagera Mahona Njigela amesema wakala huo unakadiriwa kutumia Sh.bilioni 23.7 kwa mwaka wa fedha 2026/2027 kwa ajili ya matengenezo ya aina mbalimbali ya barabara , vivuko  na madaraja ili kusogeza huduma ya usafirishaji kwa wananchi.

Wakati huo huo kupitia  kikao hicho Mkuu wa Mkoa Mkoa wa Kagera Kanali  Yahya Ramadhan Kido amewaagiza TANROADS na TARURA mkoani humo kuzingatia na kutoa kipaumbele katika masuala ya ajira kwa vijana na wanawake wakati wa utekelezaji wa miradi mbalimbali inayoendelea  na inayotarajiwa kutekelezwa.

Pia amewataka TANROADS na TARURA kuzingatia usimamizi mathubuti wa raslimari fedha kwa maana asilimia ya kazi lazima ionekane thamani yake,ubora wa kazi kwa barabara zinazojengwa au kutengenezwa zidumu kuendana na matarajio na ushirikishwaji wa wananchi katika kulinda miundombinu ya barabara.

Kikao hicho kimeudhuriwa na wabunge wa Mkoa wa Kagera ambao wamesema wataongeza nguvu kwa serikali kwa ajili ya kuleta fedha ya barabara kwani mipango ya watendaji ni mizuri changamoto  ni fedha haziji kwa wakati katika miradi ya barabara.



Top News