Wananchi wa Jiji la Dar es Salaam wanatarajiwa kushuhudia uzinduzi wa kampeni maalum ya kitaifa ijulikanayo kama Muungano Caravan, yenye lengo la kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa Muungano wa Tanzania pamoja na kuhamasisha uzalendo, mshikamano wa kitaifa na ushiriki wa wananchi katika maendeleo ya nchi.

Uzinduzi huo unatarajiwa kufanyika katika maeneo mbalimbali ya Dar es Salaam, huku mamia ya wananchi, vijana, viongozi wa serikali, wadau wa maendeleo, wanafunzi pamoja na makundi mbalimbali ya kijamii wakitarajiwa kushiriki kwa wingi katika shughuli hiyo muhimu ya kitaifa.

Kwa mujibu wa waandaaji wa kampeni hiyo, Muungano Caravan ni jukwaa maalum litakalowakutanisha wananchi kutoka makundi tofauti ili kupata elimu kuhusu historia ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, mafanikio yaliyopatikana tangu kuanzishwa kwake, pamoja na nafasi ya wananchi katika kuuenzi na kuulinda Muungano huo kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Wadau hao wameeleza kuwa vijana ndio walengwa wakuu wa kampeni hiyo kutokana na umuhimu wa kuwajengea uelewa mpana kuhusu tunu za taifa, historia ya nchi na wajibu wao katika kudumisha amani na umoja wa Watanzania.

Kupitia maonesho mbalimbali, mijadala ya wazi, semina za elimu ya uraia na vipindi vya maswali na majibu, wananchi watapata nafasi ya kujifunza kwa kina kuhusu hatua zilizopigwa katika sekta mbalimbali kutokana na Muungano ikiwemo elimu, biashara, uwekezaji, michezo, utamaduni na maendeleo ya kijamii.

Aidha, waandaaji wamebainisha kuwa vijana wengi wamekuwa wakihitaji elimu ya kina kuhusu Muungano ili waweze kuelewa chimbuko lake, faida zake na changamoto zinazoweza kujitokeza. Kupitia kampeni hiyo, vijana watapata nafasi ya kuuliza maswali moja kwa moja kwa wataalamu na viongozi wanaohusika na masuala ya Muungano.

Mbali na elimu hiyo, washiriki watapata nafasi ya kushiriki katika Muungano Challenge, shindano maalum litakalotoa zawadi mbalimbali kwa washiriki watakaofanya vizuri katika maswali yanayohusu Muungano, uzalendo, historia ya Tanzania na masuala ya maendeleo ya taifa.

Tamasha hilo pia linatarajiwa kupambwa na burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali maarufu nchini, vikundi vya ngoma za asili, muziki wa kizazi kipya pamoja na sanaa za maonesho zitakazobeba ujumbe wa umoja, amani na uzalendo.

Katika kuhakikisha ujumbe unawafikia wananchi wengi zaidi, msafara wa Muungano Caravan utaendelea katika wilaya mbalimbali za Dar es Salaam zikiwemo Ilala, Temeke, Kinondoni, Kigamboni na Ubungo. Kila eneo litakuwa na programu maalum za elimu, burudani na ushiriki wa wananchi ili kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa Muungano katika maendeleo ya taifa.

Akizungumza kuhusu kampeni hiyo, mmoja wa waratibu alisema kuwa dhamira kuu ni kujenga kizazi chenye uelewa wa historia ya taifa lao na kinachothamini amani, umoja na mshikamano uliopo nchini.

“Tunataka vijana wawe mstari wa mbele katika kuujua na kuuenzi Muungano wetu. Elimu hii ni muhimu kwa sababu vijana ndio viongozi wa kesho, hivyo wanapaswa kuelewa mchango wa Muungano katika kulinda amani na kuleta maendeleo ya taifa letu,” alisema.

Aidha, viongozi mbalimbali wa kijamii na wadau wa maendeleo wamepongeza kuanzishwa kwa kampeni hiyo wakisema kuwa itasaidia kuimarisha mshikamano wa kitaifa na kuongeza uelewa kwa wananchi kuhusu masuala ya Muungano ambayo kwa muda mrefu yamekuwa yakihitaji elimu zaidi hasa kwa kizazi cha vijana.

Kaulimbiu ya kampeni hiyo ni:
“Safari ya Umoja – Tudumishe Muungano Wetu kwa Maendeleo Endelevu.”

Wananchi wametakiwa kujitokeza kwa wingi kushiriki katika uzinduzi huo ambao unatarajiwa kuwa mwanzo wa harakati mpya za kuendeleza uzalendo, elimu ya uraia na mshikamano wa kitaifa nchini Tanzania.




 





Waziri wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (Mb), leo tarehe 6 Mei, 2026 amefungua rasmi Mkutano Mkuu wa Pili wa Mwaka wa Jumuiya ya Wataalamu wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu katika Utumishi wa Umma (AAPAM), unaowakutanisha wadau mbalimbali wa sekta hiyo.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano huo uliofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC), Waziri Ridhiwani alisisitiza umuhimu wa wataalamu wa Rasilimali watu katika kuimarisha utendaji na ufanisi wa taasisi za umma ambapo alibainisha kuwa mchango wao ni muhimu katika kufanikisha utoaji wa huduma bora ili kuendana na kasi ya mabadiliko ya kiutawala na kiteknolojia.

Aidha, alieleza kuwa Serikali inaendelea kuweka mazingira rafiki kwa wataalamu hao ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa weledi.


Katika ziara yake katika mabanda ya maonesho yanayoambatana na mkutano huo, Mhe. Ridhiwani alitembelea banda la Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), ambapo alipata fursa ya kujionea shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na taasisi hiyo pamoja na maboresho ya huduma zake.


Meneja Masoko na Uhusiano kwa Umma TEMESA Bi Martha Joachim akimkabidhi zawadi Waziri wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (Mb)



Akiwa katika banda hilo, aliipongeza TEMESA kwa kumpata Mtendaji Mkuu mpya, nakusema hatua hiyo imeashiria fursa ya kuimarisha zaidi uongozi, kuongeza ubunifu na kuleta matokeo chanya katika utoaji wa huduma kwa umma.


“TEMESA kwanza nawapongeza kwa kupata mtendaji mpya naamini mabadiliko haya yataleta chachu ya kiutendaji na utoaji wa huduma bora hongereni sana.” Amesema Mhe. Ridhiwani.


Mkutano huo wa siku nne umebeba kaulimbiu isemayo: “Kufikiri upya utoaji wa huduma kwa umma: Jinsi Serikali inavyoweza kutumia teknolojia kuanzisha huduma bora na zinazomlenga mwananchi, kukabiliana na ukosefu wa ajira kwa vijana pamoja na changamoto za mazingira.”

Meneja wa Kanda Namba Sita, Halmashauri ya Jiji la Dodoma Lucas Nkelege amekutana na watendaji wa kata pamoja na watendaji wa mitaa inayounda kanda hiyo kwa lengo la kutoa elimu ya vyanzo vya mapato na kuwakumbusha umuhimu wa ukusanyaji wa mapato kwa wakati ili kuongeza ufanisi wa huduma kwa wananchi.

Akizungumza katika kikao hicho, Nkelege ameeleza kuwa mapato yanayokusanywa katika maeneo mbalimbali ndiyo msingi wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo pamoja na kuboresha huduma muhimu za jamii ikiwemo usafi wa mazingira, ujenzi wa miundombinu na huduma za kijamii.

Amesisitiza kuwa watendaji wanapaswa kuwa mstari wa mbele katika kutoa elimu kwa wananchi kuhusu ulipaji wa tozo na ada mbalimbali kwa hiari na kwa kuzingatia taratibu zilizowekwa, huku akiongeza kuwa ukusanyaji wa mapato ni jukumu la pamoja linalohitaji ushirikiano wa karibu kati ya watendaji wa kata, mitaa na viongozi wa serikali za mitaa. 

“Ukusanyaji wa mapato si kazi ya mtu mmoja, ni jukumu la pamoja. Tukishirikiana kwa karibu, tutakusanya mapato kwa ufanisi na kuleta maendeleo ya haraka kwa wananchi wetu” alisema Nkelege.

Watendaji wanahimizwa kutambua na kusimamia vyanzo vyote vya mapato vilivyopo kwenye maeneo yao ikiwemo biashara ndogondogo, ushuru wa huduma, ada za vibali na vyanzo vingine halali vya mapato ili kuzuia upotevu wa mapato.







Nimezungumza na maafisa tawala na RasilimaliWatu , katika mkutano uliofanyika Ukumbi wa AICC, Arusha na kuwakumbusha kutekeleza wajibu wao na kuleta furaha kwa watumishi wa umma ili kwa upande mwengine nao wapeleke furaha na neema kwa Watanzania . Nimeyaeleza hayo kufuatia maamuzi mbalimbali yanayofanywa na serikali ya awamu ya sita katika kuhakikisha maslahi ya Watumishi wa umma nchini yanaboreka.

Uamuzi wa hivi karibuni wa Serikali kupandisha madaraja watumishi 219,042 ni hatua ya kihistoria katika kuimarisha utumishi wa umma nchini Tanzania. Hatua hii ambayo imepata ridhaa ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na ongezeko la mishahara ya watumishi wa umma (2025): +35.1% , Ongezeko la kima cha chini sekta binafsi (2025/26): +33.4% , ambapo Sekta mbalimbali zinakwenda athiriwa na maboresho haya ikiwemo afya, elimu, kilimo, mawasiliano, usafirishaji, nishati, viwanda, biashara, hoteli, michezo, uvuvi, baharini, madini ,utamaduni n.k

Matokeo haya kitakwimu zinaonyesha kasi ya mageuzi ya kiutumishi chini ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan ambayo inaonyesha uongozi wa kimkakati unaoweka mbele ustawi wa watumishi na ufanisi wa taasisi za umma.





📍 Apandisha mishahara kwa asilimia 35


Na Mwandishi Wetu, Arusha

SERIKALI ya Awamu ya Sita imefanya mageuzi makubwa ya kiutumishi nchini kwa kupandisha madaraja watumishi wa umma 219,042, huku ikiongeza mishahara kwa asilimia 35.1, hatua inayotajwa kuwa ni kielelezo cha uongozi unaoweka mbele ustawi wa mfanyakazi.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete, ameyabainisha hayo leo jijini Arusha wakati akizungumza na Maafisa Tawala na Rasilimali Watu katika mkutano uliofanyika Ukumbi wa AICC.

Mhe. Kikwete alisema maamuzi hayo ya kimkakati yaliyopata ridhaa ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, yanalenga kuleta "furaha na neema" kwa watumishi wa umma ili nao waweze kutoa huduma bora na kupeleka furaha kwa Watanzania wote kupitia utendaji wao.

Ongezeko la Mishahara na Sekta Binafsi

Akifafanua kuhusu neema hiyo ya kiutumishi, Waziri Kikwete alibainisha kuwa mbali na ongezeko la 35.1% kwa watumishi wa umma mwaka 2025, Serikali pia imeimarisha sekta binafsi kwa kuongeza kima cha chini cha mishahara kwa 33.4% kwa mwaka wa fedha 2025/26.

Alisema maboresho hayo yanagusa sekta mbalimbali za kimkakati nchini ikiwemo Afya, Elimu, Kilimo, Mawasiliano, Usafirishaji, Nishati, Viwanda, Biashara, Madini, na Utalii.

"Nimezungumza na maafisa rasilimali watu na kuwakumbusha kutekeleza wajibu wao wa kuleta furaha kwa watumishi. Uamuzi wa Rais Samia kupandisha madaraja watumishi zaidi ya laki mbili ni hatua ya kihistoria katika kuimarisha utumishi wa umma nchini Tanzania," alisema Waziri Kikwete.

Waziri Kikwete aliongeza kuwa takwimu hizo zinaonyesha kasi ya mageuzi chini ya uongozi wa Rais Samia, ambaye amedhihirisha kwa vitendo kuwa ufanisi wa taasisi za umma unategemea sana kuimarika kwa maslahi na hali ya maisha ya watumishi.

Aliwataka Maafisa Tawala nchini kuhakikisha wanatekeleza maelekezo ya Serikali kwa uadilifu ili watumishi wapate haki zao kwa wakati, jambo litakaloongeza morali ya kazi na tija katika kuwahudumia wananchi.





Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na shirika la kimataifa la Brooke East Africa, inatarajia kuhitimisha kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Punda Kitaifa hapo kesho.

Hafla hiyo ya kimkakati imepangwa kufanyika katika Kata ya Mgusu, iliyopo ndani ya Halmashauri ya Manispaa ya Geita, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kitaifa za kutambua mchango wa mnyama huyu katika uchumi.

Uamuzi wa kuifanya Kata ya Mgusu kuwa kitovu cha maadhimisho haya umechangiwa na takwimu za kijiografia na kiuchumi zinazoonyesha mwingiliano mkubwa kati ya jamii na punda.

Afisa Mifugo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bi. Tabitha Kitingu, amebainisha kuwa eneo hilo lina idadi kubwa ya punda ambao ni kiungo muhimu katika mnyororo wa uzalishaji, hususan kwenye shughuli za uchimbaji madini.

Kwa mujibu wa tathmini za kitaalamu, Kata ya Mgusu pekee inakadiriwa kuwa na idadi inayozidi Punda 500.

Kutokana na idadi hiyo kubwa, Serikali imeona umuhimu wa kutoa kipaumbele katika utoaji wa elimu ya kina kwa wamiliki na watumiaji wa wanyama hao, lengo likiwa ni kuhakikisha punda wanapata huduma bora na stahiki kulingana na miongozo ya ustawi wa wanyama duniani.

Msingi mkuu wa maadhimisho haya ni kusisitiza haki za msingi za mnyama kazi, ambazo mara nyingi hupuuzwa kutokana na shinikizo la shughuli za kiuchumi migodini.

Elimu itakayotolewa inalenga kubadilisha mitazamo ya wafugaji ili wajali afya, lishe, na mapumziko ya punda, jambo ambalo ni muhimu katika kuongeza tija na uendelevu wa nguvu kazi ya mnyama huyo.

Kwa upande wake, Daktari wa Mifugo kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Geita, Dkt. David Misonge, amethibitisha kuwa wataalamu wa afya ya wanyama wamekusanywa kutoka maeneo mbalimbali mkoani humo.

Kikosi hicho cha wataalamu kimejipanga kutoa huduma za kitabibu na ushauri wa kitaalamu, hasa katika maeneo ya migodi ambapo punda hukabiliwa na changamoto nyingi za kiafya kutokana na kubeba mizigo mizito.

Maadhimisho haya pia yanajumuisha zoezi la uchunguzi wa afya na matibabu ya punda wenye magonjwa na majeraha mbalimbali yanayotokana na mazingira yao ya kazi.

Hatua hii ni sehemu ya mkakati mpana wa Serikali mkoani Geita wa kudhibiti maradhi ya mlipuko miongoni mwa mifugo na kuhakikisha kuwa mnyama kazi hapati mateso yasiyo ya lazima wakati wa utekelezaji wa majukumu yake.

Aidha, Serikali imesisitiza dhamira yake ya dhati ya kuendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo katika kutoa elimu endelevu kwa wananchi.

Lengo ni kujenga jamii yenye uelewa wa kisheria na kimaadili kuhusu utunzaji wa wanyama, ili kuondoa kabisa vitendo vya ukatili na kuhakikisha punda wanatibiwa kwa wakati wanapougua.

Kwa upande mwingine, jamii ya wafugaji na wakazi wa Geita wametoa shukrani zao za dhati kwa mashirika ya Brooke East Africa na ASPRA kwa mchango wao thabiti.

Mashirika haya yamekuwa mstari wa mbele katika kutoa matibabu ya ruzuku na mafunzo ya mbinu bora za ufugaji, hali inayochochea mabadiliko chanya ya kijamii na kiuchumi katika mkoa wa Geita.





Serikali itaendelea kuimarisha usimamizi na maendeleo ya taaluma ya ualimu nchini kupitia utekelezaji wa majukumu ya Bodi ya Kitaalamu ya Walimu Tanzania (Tanzania Teachers Professional Board), ikiwa ni sehemu ya juhudi za kulinda na kuinua hadhi ya taaluma hiyo.

Kupitia hatua hiyo, Serikali itaandaa mwongozo wa viwango vya ufundishaji ili kukuza mafunzo endelevu kwa walimu, pamoja na kuandaa Mwongozo wa Maadili na Mwenendo wa Taaluma ya Ualimu utakaosaidia kuimarisha nidhamu na weledi katika sekta ya elimu.

Hayo yameelezwa bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara yake kwa mwaka wa fedha 2026/27.

Katika hatua nyingine, Serikali itaanza kutekeleza mpango wa mafunzo kwa vitendo wa mwaka mmoja (internship) kwa wahitimu wa mafunzo ya ualimu, hatua inayolenga kuwawezesha walimu tarajali kuoanisha maarifa ya nadharia na uhalisia wa kazi darasani.

Aidha, Serikali itaendelea kuwajengea uwezo walimu wa shule za msingi na sekondari, wakufunzi wa vyuo vya ualimu, wathibiti ubora wa shule na wasimamizi wa elimu ili kuboresha utendaji katika sekta ya elimu.

Katika mpango huo, walimu 1,223 watanufaika na ufadhili wa masomo ya Stashahada ya Ualimu wa Elimu Maalum, huku walimu 3,000 wakipatiwa mafunzo ya ushauri na unasihi kuhusu malezi, stadi za maisha na ulinzi wa mtoto.

Vilevile, watendaji 5,500 pamoja na walimu na wanafunzi watanufaika na mafunzo kuhusu matumizi ya majukwaa ya kielimu, ikiwemo maktaba mtandao na majukwaa ya kujifunza mtandaoni kwa lengo la kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika elimu.



WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa Kikao Kazi cha 21 cha Maafisa Habari, Mawasiliano, Itifaki na Uhusiano Serikalini Mei leo 7, 2026 mkoani Njombe.

Kikao kazi hicho cha mwaka, kinawakutanisha zaidi ya Maafisa Habari 300 kutoka taasisi mbalimbali za Serikali kote nchini kwa lengo la kuwanoa na kuwajengea uwezo, kusimamia na kuzifikisha kwa ufanisi taarifa za Serikali kwa umma.

Kupitia kikaokazi hicho washiriki watapata mafunzo na kufanya mijadala mizito ikiwemo ya uandishi wa kisasa wa taarifa kwa umma, mbinu za kuandika makala zenye mvuto magazetini pamoja na kanuni muhimu za itifaki katika shughuli za kitaifa.

Aidha, watapata fursa ya kujifunza kuhusu matumizi sahihi ya picha za viongozi, utaratibu wa utajo rasmi na suala la mwonekano wa mavazi katika mikutano ya kitaifa na kimataifa

Katika hatua ya kuimarisha mawasiliano ya Serikali hadi ngazi za chini, washiriki wameendelea kuhimizwa kushirikiana kwa karibu na redio za kijamii pamoja na klabu za waandishi wa habari mikoani ili kuongeza ufanisi wa utoaji wa taarifa kwa wananchi.

Sambamba na kikao hicho, wananchi wa Mkoa wa Njombe wananufaika na huduma za kibingwa bobezi zinazotolewa na wataalamu kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili (Upanga na Mloganzila) pamoja na Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Ubongo Muhimbili (MOI).

Mbali na mafunzo hayo, washiriki pia watapata fursa ya kutembelea kiwanda cha AVO AFRICA kinachozalisha mafuta ya parachichi, kushuhudia vivutio vya asili ikiwemo maporomoko ya maji ya Mpanga Kipengele, na kushiriki zoezi la upandaji miti kulinda vyanzo vya maji katika Halmashauri ya Mji wa Njombe.

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan aongoza Kikao cha kawaida cha Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kilichoketi mkoani Dodoma tarehe 07 Mei 2026.

 

Na Mwandishi Wetu, Nairobi

Rais wa Kenya, William Ruto, amempongeza Jaji Mohammed Abdullahi Warsame baada ya kuapishwa rasmi kuwa jaji wa 14 wa Mahakama ya Juu ya Kenya, akieleza kuwa uzoefu wake mkubwa utasaidia kuimarisha utoaji wa haki nchini humo.

Akizungumza katika hafla iliyofanyika Ikulu ya Nairobi, Rais Ruto alisema ana imani kuwa Jaji Warsame ataleta mchango chanya katika mahakama hiyo ya juu kabisa nchini Kenya kupitia weledi na uzoefu wake wa muda mrefu katika sekta ya sheria.


 “Unaungwa mkono kikamilifu na tunakuombea mafanikio unapoanza jukumu hili muhimu la kulitumikia taifa letu,” alisema Ruto wakati wa hafla ya kuapishwa kwa jaji huyo.

Katika hafla hiyo pia, Rais Ruto aliwapongeza Evans Thiga Gaturu na Jedidah Wakonyo Waruhiu baada ya kutunukiwa hadhi ya Senior Counsel, akisema wameonyesha mchango mkubwa katika kuimarisha utawala wa sheria na demokrasia ya kikatiba nchini Kenya.

Ruto alisema Serikali ya Kenya itaendelea kushirikiana na mihimili mingine ya dola kuhakikisha haki inatendeka na mfumo wa sheria unaendelea kuimarika kwa manufaa ya wananchi wote.

Hafla hiyo ilihudhuriwa pia na Naibu Rais wa Kenya, Kithure Kindiki pamoja na Jaji Mkuu na Rais wa Mahakama ya Juu Kenya, Martha Koome.







Uongozi wa Taasisi ya LALJI FOUNDATION ukiwa katika picha ya pamoja na wanachama wa Chama cha Wanawake Wajane Tanzania (CCWWT) mkoani Kigoma mara baada ya kukabidhi mizinga 50 ya nyuki, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuwawezesha wajane kiuchumi kupitia ufugaji nyuki.

KATIKA juhudi za kuwawezesha wanawake wajane kujikwamua kiuchumi, Taasisi ya LALJI FOUNDATION imekabidhi mizinga 50 ya nyuki kwa Chama cha Wanawake Wajane Tanzania (CCWWT) mkoani Kigoma, ikiwa ni sehemu ya mpango wa kukuza kipato kupitia ufugaji nyuki.

Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano hayo, Katibu wa LALJI FOUNDATION, Bi. Fatema Imtiaz Lalji, amesema kuwa huo ni mwanzo wa utekelezaji wa mpango mkubwa unaolenga kugawa jumla ya mizinga 200 kwa wajane katika maeneo mbalimbali nchini.

Amesema taasisi hiyo imeanza na mkoa wa Kigoma kwa kuwalenga wajane, ambao mara nyingi hukumbana na changamoto za kiuchumi na kijamii, hivyo kuwapatia fursa ya kujipatia kipato kupitia ufugaji nyuki.

“Tunatambua mchango wa wanawake katika jamii, lakini pia tunatambua changamoto wanazokutana nazo, hususan wajane. Kupitia mradi huu, tunalenga kuwapa uwezo wa kujitegemea kiuchumi,” amesema Bi. Lalji.

Ameongeza kuwa zoezi hilo litakuwa endelevu, huku taasisi hiyo ikiendelea kufikia makundi mbalimbali yenye uhitaji katika maeneo tofauti nchini.

Amesema Kabla ya kukabidhi mizinga hiyo LAJI FOUNDATION iliendesha mafunzo ya kitaalamu kwa wanufaika wa mradi huo ambayo yalifanyika Febuari 15, 2026 Wilayani Bagamoyo ili kuhakikisha wanapata ujuzi sahihi wa utunzaji wa mizinga, uvunaji wa asali kwa njia salama, pamoja na uhifadhi wa bidhaa zitokanazo na nyuki.

“Mafunzo hayo yatasaidia kuongeza tija na ubora wa mazao, hivyo kuwawezesha wajane hao kushindana katika soko”

Ameongeza kuwa pamoja na kugawa mizinga, pia kuna mpango wa kuwasaidia wanufaika kupata masoko ya uhakika ya bidhaa zao, ikiwemo asali na nta, ili kuhakikisha wanapata faida stahiki. Hatua hiyo inalenga kuondoa changamoto ya soko ambayo imekuwa ikiwakwamisha wafugaji wengi wadogo nchini.

Kwa upande wao, wanachama wa CCWWT mkoani Kigoma wameishukuru LALJI FOUNDATION kwa msaada huo, wakisema utasaidia kubadilisha maisha yao na kuongeza kipato cha familia.

Wamesema ufugaji nyuki ni fursa muhimu inayoweza kuleta maendeleo endapo watapatiwa elimu na usimamizi mzuri, huku wakiahidi kuitunza na kuitumia vizuri mizinga hiyo ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Mradi huo unatarajiwa kuwa chachu ya maendeleo kwa wajane hao, huku ukichangia pia katika uhifadhi wa mazingira na uzalishaji wa mazao ya nyuki kama asali, nta na bidhaa nyingine zitokanazo na nyuki

Top News