Na Mwandishi Wetu, Tanga.

Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) imewezesha ziara ya mafunzo kwa Viongozi wa Mila (Malaigwanani), Wazee Mashuhuri na kinamama  33 kutoka kata 11 za tarafa ya Ngorongoro kutembelea kiwanda cha kuzalisha na kuchakata mazao ya maziwa cha Tanga Fresh, kilichopo jijini Tanga.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mwenyekiti wa Malaigwanani Ngorongoro na Diwani wa Kata ya Olbalbal, Mhe. Metui Shaudo alisema, ziara hiyo imewapa fursa ya kuona kwa vitendo hatua mbalimbali zinazofanyika katika uchakataji wa maziwa, kuanzia ukusanyaji wa maziwa, uzalishaji na uuzaji wa bidhaa mbalimbali zilizoongezewa thamani.

 “Tumetembelea kiwanda hiki kujifunza na kuona mambo mengi ambayo tunaweza kuyatumia tunaporudi Ngorongoro, tumeona kuwa maziwa yanaweza kuwa na thamani kubwa zaidi yakichakatwa vizuri badala ya kuuzwa yakiwa ghafi kama ambavyo mara nyingi inafanyika kwa wananchi wetu, baada ya ziara hii tutapelekeaa elimu hii kwa wananchi wenzetu ili kuwaongezea tija na kipato kinachotokana na ufugaji,” alisema Mhe. Shaudo 

Kina mama walioshiriki ziara hiyo  wameelezea kufurahishwa na manufaa yanayotokana na  mifugo na kuwaongezea ujuzi wa uchakataji na uongezaji thamani wa mazao ya mifugo na kuahidi kutoa elimu hiyo kwa wananchi wa Ngorongoro ili waendelee kujikwamua kiuchumi.

Kiongozi wa mila kutoka kata ya kakesio Ole Kotika ameeleza kuwa ziara hiyo  inaendelea kuimarisha mahusiano mazuri kati ya hifadhi ya Ngorongoro na wananchi hasa kuwaongezea fursa ya kujifunza shughuli za ufugaji wa kisasa, usindikaji wa bidhaa za maziwa zenye ubora na kuongeza mnyororo wa thamani ambao unasaidia kukuza uchumi wa wananchi.

Ziara ya viongozi hao ni sehemu ya jitihada za Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kupitia Idara ya Maendeleo ya Jamii ya kuwawezesha wananchi wanaoishi ndani ya hifadhi ya Ngorongoro kupata ujuzi na uzoefu unaoweza kuboresha shughuli zao za kiuchumi na kuongeza thamani ya rasilimali walizonazo.










Na HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amesema kuwa, Haki Jinai si mali ya Taasisi moja bali ni mfumo wenye Taasisi nyingi, wenye lengo la kuhakikisha haki inapatikana mapema ipasavyo kwa usawa, uadilifu na kwa kuzingatia Katiba na Sheria za nchi huku akieleza kuwa wadau wote wanapaswa kushirikiana kwa pamoja ili kuhakikisha haki haicheleweshwi bila sababu za msingi.

Mhe. Masaju ameyasema hayo wakati wa kufunga Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani leo tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

“Haki jinai ni mfumo mmoja wenye taasisi nyingi lakini wenye lengo moja, yaani kuhakikisha kuwa haki inapatikana mapema ipasavyo tunapaswa kuzungumza kuhusu mfumo mzima kwa sababu udhaifu wa kiungo kimoja katika mnyororo wa haki jinai unaweza kuchelewesha haki kwa mfumo mzima,” amesema Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju ametoa mfano wa Mtume Paulo anapozungumza kuhusu kanisa ambapo amesema, “ni kama mwili wa binadamu, kama ambavyo kuna mikono, macho, miguu, lakini hivyo vyote ndiyo vinakamilisha mwili. Yaani macho hayawezi kujifanya yenyewe ni bora kuliko mguu na vile viungo vilivyoonekana kama ni dhaifu, hivyo Mungu alivifanya kuwa vya maana zaidi lakini ukweli hapa wote hakuna kiungo dhaifu, hizi Taasisi zote ni muhimu.”

Ameongeza kuwa, jukumu la kwanza la sheria duniani kote ni kusimamia utawala wa sheria, amani na usalama katika jamii na jukumu la pili ni kukusanya kodi kwa ajili ya maendeleo mbalimbali na kuongeza kuwa hata Mwenyezi Mungu huko mbinguni aliweka sheria, na aliyekwenda kinyume na sheria aliwajibika kama ambavyo Lucifer alivyowajibika.

“Kwa hiyo, mkishakuwa zaidi ya mtu mmoja tu lazima mjiwekee sheria namna ya kufanya mambo yenu na kwetu Tanzania utawala wa sheria unapatikana katika Ibara ya 26 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na mfumo wowote lazima uwe unaongozwa na utawala wa sheria, hata Mwenyezi Mungu kule mbinguni aliweka sheria, na bwana mkubwa yule akiitwa Lucifer alipoasi akawajibika” amesema Mhe. Masaju.

Katika hatua nyingine Jaji Mkuu amefafanua kuwa, Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 inasisitiza juu ya amani, usalama na utulivu, ulinzi wa haki, uhuru wa msingi, uimara wa Taasisi na utawala wa sheria ambao ni kipengele muhimu cha utawala bora kinachosaidia kujenga jamii yenye usawa, uwajibikaji, haki na kuaminiana.

Aidha, ameeleza kuwa, mashauri ya jinai hayaanzii mahakamani wala polisi pekee kwa kuwa vyombo hivyo vyote haviwi sehemu na wakati ambapo matukio hayo ya kihalifu yanatokea hivyo, wadau wote wanapaswa kuungana na kufanya kazi kwa pamoja kama ambavyo viungo katika mwili vinavyofanya kazi kwa pamoja na kutegemeana.

“Kesi ya jinai inaanza kwenye jamii huko tukio linapotokea, inaenda kwenye vyombo vya uchunguzi iwe ni Polisi, ni Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, ni Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, inaenda Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, hatimaye kama kuna ushahidi inaenda mahakamani, na waliohusika kumkamata mshukiwa wanakuja kutoa ushahidi mahakamani kama amepatikana na hatia anarudi gerezani kwa ajili ya reform, utaona kwamba huu mnyororo ni mpana ni mnyororo mrefu lakini mnyororo imara, ” ameeleza Mhe. Masaju.

Katika hatua nyingine, amesema kuwa, ni vema kukawa na mtiririko mzuri wa kimfumo wa usimamizi wa mashauri ya jinai ili kuondoa changamoto zinazokwamisha mashauri kumalizika na kuongeza kuwa Mahakama haiwezi kuwa na ufanisi wa asilimia 100, ikiwa hatua zilizotangulia hazifanyi kazi mapema ipasavyo na kwa ufanisi na kwamba kunaweza kuwa na Mahakama yenye uwezo wa kusikiliza Mashauri Majaji na Mahakimu wenye uwezo lakini kama uchunguzi haujakamilika au kuwepo kwa changamoto yoyote shauri haliwezi kuendelea.

“Mahakama haiwezi kuwa na ufanisi wa asilimia 100 ikiwa hatua zilizotangulia Mahakama hazifanyi kazi mapema ipasavyo na kwa ufanisi. Tunaweza kuwa na Mahakama yenye uwezo wa kusikiliza mashauri, Majaji na Mahakimu wenye uwezo, na mifumo ya kielektroniki au miundombinu, lakini pia ni waadilifu. Lakini kama uchunguzi haujakamilika, jalada halijawasilishwa, mashahidi hawapatikani, maelezo hayajakamilika, hati za mashtaka zina kasoro, mshtakiwa hajaletwa mahakamani, au nyaraka muhimu hazijafikishwa mahakamani mapema, katika mtiririko kama huu kesi haiwezi kwenda mbele, hivyo ni vema kukawa na ile systematic flow ya criminal justice ya case management ili kuondoa hizo changamoto” amesisitiza Jaji Mkuu.

Akizungumza kuhusu uwajibikaji na kujituma, Mhe. Masaju amesema kuwa, kila Taasisi ya Haki Jinai inapaswa kuwajibika ipasavyo ili kuondoa ucheleweshaji wa mashauri bila kusubiri shauri lifike mahakamani huku akirejea Ibara ya 25 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inasisitiza juu ya uwajibikaji na kujituma katika kila kazi kwa kufahamu chanzo cha kukwama kwa shauri, wapi lilipofikia katika utekelezaji, imefikia hatua zipi za ushahidi, jambo litakalosaidia mnyororo mzima wa haki jinai kufanya kazi vizuri.

Kadhalika, Mhe. Masaju amewakumbusha wadau wa Haki Jinai kwamba, mfumo unahitaji ushirikiano thabiti, mawasiliano ya karibu na uratibu mzuri ambayo ndio nguzo ya mafanikio hivyo, taasisi zote zifanye kazi bila kujitenga.

“Ni vyema tukumbuke kuwa, mfumo wetu wa haki jinai unahitaji ushirikiano thabiti (cooperation), mawasiliano ya karibu (communication), na uratibu mzuri (coordination). Hivi vitu vitatu yaani Cooperation, Communication, and Coordination ndivyo nguzo kuu za mafanikio yetu katika usimamizi wa haki jinai. Kama taasisi moja inafanya kazi kwa kujitenga au bila kutoa taarifa kwa nyingine, ni wazi kuwa, kutakuwa na kukwama kwa mashauri au kuchelewa kwa haki,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Kadhalika, Mhe. Masaju amezitaka Taasisi za mnyororo wa Haki Jinai kuzingatia matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) na kuhakikisha mifumo inasomana ili kurahisisha mchakato mzima wa kuhakikisha haki inapatikana mapema ipasavyo bila kucheleweshwa na sababu zisizo na msingi.

Akihitimisha hotuba yake. Mhe. Masaju amezitaka Taasisi za mnyororo wa Haki Jinai kuchukua tahadhari juu ya uwepo wa mvua za El nino kwa kuhakikisha wanaweka miundombinu imara itakayowawezesha kufanya kazi pindi mvua hizo zitakapoanza kunyesha.
Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Majaji, Viongozi na Watumishi wa Mahakama pamoja na Wadau wa Haki Jinai wakati wa Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Aliyeketi kushoto ni Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma na kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa hotuba ya kufunga Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.





Baadhi ya Viongozi, Watumishi wa Mahakama pamoja na Wadau wa Haki Jinai wakisikiliza hotuba ya Jaji Mkuu alipokuwa akifunga Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma akitoa neno wakati wa kufunga Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya akitoa taarifa ya utekelezaji wa mikakati kwa upande wa Mahakama wakati wa Mkutano kati ya Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


(Picha na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo imesema haitambui matamko yanayohusu jezi mpya za timu za taifa, ikieleza kuwa mchakato wa kubadilisha jezi hizo haukuishirikisha Wizara licha ya maelekezo yaliyotolewa mwezi Februari 2026.

Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa na Wizara hiyo leo September 18, 2026 imesema Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Christian Makonda, ameeleza kuwa Serikali inawekeza fedha nyingi katika maandalizi ya timu za taifa zinazoshiriki mashindano ya kimataifa.

Taarifa hiyo imeongeza kuwa, kwa kuzingatia Tanzania kuwa mwenyeji wa mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027, kuna umuhimu wa kuboresha jezi za timu za taifa ili ziakisi manufaa mapana kwa nchi.

Aidha, Wizara imesema Waziri Makonda ataandaa Kamati ya kuchunguza mkataba wa mzabuni wa jezi za timu za taifa, kwa lengo la kubaini manufaa yanayotokana na mkataba huo kwa timu hizo.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, hatua hiyo inazingatia ukweli kwamba Serikali imekuwa ikitumia fedha nyingi kuendesha timu za taifa, huku kukiwa na fursa ya mauzo ya jezi ambazo zinaweza kuchangia katika uendeshaji wa timu hizo.





 Na Mwandishi Wetu, Arusha

HOSPITALI ya JKCI–ALMC Arusha (Selian ya Mjini) imeandaa Kambi Maalum ya Matibabu ya Kibingwa itakayofanyika kuanzia Septemba 21 hadi 24, 2026, ikiwakutanisha madaktari bingwa na wabobezi kutoka Tanzania na India.

Mkurugenzi wa Hospitali hiyo, Dkt. Tatizo Waane, alisema jana kuwa kambi hiyo itawakutanisha wataalamu kutoka Apollo Hospitals–India, Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Taasisi ya Mifupa Muhimbili (MOI), Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) pamoja na madaktari bingwa wa JKCI–ALMC Arusha.

Dkt. Juma Magogo Mzimbiri,, Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo, Uti wa Mgongo na Mfumo wa Fahamu kutoka MOI,

Alisema kambi hiyo imelenga kuwafikishia wananchi huduma za kibingwa katika maeneo ya magonjwa ya mfumo wa fahamu, upasuaji wa ubongo na uti wa mgongo, magonjwa na upasuaji wa mfumo wa mkojo, pamoja na magonjwa, upasuaji wa mifupa, viungo na majeraha.

“Tunatarajia kuona wagonjwa kati ya 100 hadi 200 kwa siku. Watapata nafasi ya kuonana na madaktari bingwa, kufanyiwa tathmini, kupata ushauri wa kitaalamu na kuelekezwa kuhusu hatua zinazofaa za matibabu,” alisema Dkt. Waane.

Dkt. Mahendra Pal, Daktari Bingwa wa Saratani za Mfumo wa Mkojo (Uro-Oncology) kutoka Apollo Hospitals, Mumbai, India.

Alisema huduma zitakazotolewa moja kwa moja kupitia kambi hiyo zitakuwa bila malipo, lakini mgonjwa atakayehitaji vipimo, dawa, upasuaji au huduma nyingine za ziada atachangia gharama kulingana na huduma inayohitajika.

Kwa mujibu wa Dkt. Waane, baadhi ya wagonjwa watakaobainika kuwa na matatizo yanayohitaji matibabu ya kina wataandaliwa kwa ajili ya upasuaji au huduma nyingine za kibingwa kulingana na tathmini ya madaktari. Alitoa wito kwa wananchi wa Arusha na mikoa jirani, ikiwemo Kilimanjaro, Manyara, Singida na maeneo mengine ya Kanda ya Kaskazini, kutumia fursa hiyo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Tiba wa JKCI–ALMC Arusha na Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo, Dkt. Salehe Hamisi Mchete, alisema kambi hiyo ni sehemu ya juhudi za kusogeza huduma za kibingwa na ubingwa bobezi karibu zaidi na wananchi.

Alisema pamoja na kutoa huduma kwa wagonjwa, kambi hiyo itatumika kujenga uwezo wa wataalamu wa afya kupitia Mafunzo Endelevu ya Kitabibu (CME) yatakayoshirikisha madaktari bingwa kutoka Tanzania na India.

“Tunataka baada ya kambi hii wagonjwa wapate huduma, lakini pia maarifa yabaki kwa wataalamu wetu. Tutajadili mbinu za kisasa za matibabu, teknolojia mpya za upasuaji na namna bora zaidi ya kuwahudumia wagonjwa,” alisema Dkt. Mchete.

Akizungumza kwa niaba ya timu ya madaktari kutoka Apollo Hospitals–India, Dkt. Mahendra Pal, Daktari Bingwa wa Saratani za Mfumo wa Mkojo (Uro-Oncology), alisema wamefurahishwa kupata nafasi ya kuja Tanzania kufanya kazi pamoja na madaktari bingwa wa hapa nchini.

Dkt. Pal, ambaye amebobea katika saratani za tezi dume, figo, kibofu cha mkojo, korodani na saratani nyingine za mfumo wa mkojo, alisema wataalamu kutoka Apollo watashirikiana na madaktari wa Tanzania katika maeneo ya urology, neurosurgery na orthopaedics.



“Tunafurahi kuja Tanzania na kufanya kazi pamoja na wataalamu wa hapa. Tunawaalika wananchi kutumia fursa hii kuonana na madaktari waliobobea na kupata huduma zinazohitajika,” amesema.

Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo, Uti wa Mgongo na Mfumo wa Fahamu kutoka MOI, Dkt. Juma Magogo Mzimbiri, alisema ujio wa wataalamu hao ni fursa muhimu kwa wananchi wa Arusha na Kanda ya Kaskazini kupata huduma za madaktari bingwa wa ndani na nje ya nchi katika eneo moja.

Amesema katika kambi hiyo atashiriki pamoja na Dkt. Remigius Rugakingira, Daktari Bingwa wa Mfumo wa Mkojo kutoka BMH, na Dkt. Emil Urasa, Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Mifupa na Majeraha kutoka MOI.

“Tunawahimiza wananchi wenye matatizo ya uti wa mgongo, ubongo, kifafa, kiharusi na matatizo mengine ya mfumo wa fahamu kutumia fursa hii. Vilevile wenye matatizo ya mfumo wa mkojo, tezi dume, matatizo ya korodani kwa watoto na baadhi ya changamoto za figo zinazohitaji tathmini ya urology wanakaribishwa,” amesema Dkt. Magogo.


Uongozi wa JKCI–ALMC Arusha (Selian ya Mjini) umetoa wito kwa hospitali na vituo vya afya kuwaelekeza wagonjwa wanaoweza kunufaika na huduma hizo, huku taasisi za afya zikihimizwa kuwawezesha wataalamu wao kushiriki katika mafunzo ya CME.

Kambi hiyo itafanyika JKCI–ALMC Arusha (Selian ya Mjini) kuanzia Septemba 21 hadi 24, 2026.

Na. Philipo Hassan - Mikumi

Ujenzi wa uwanja wa ndege wa Kikoboga uliopo ndani ya Hifadhi ya Taifa Mikumi umefikia asilimia 75, ukihusisha jengo lenye uwezo wa kuhudumia abiria 160 kwa ujumla wanaowasili na wanaoondoka, njia ya kurushia na kutua ndege (Runway) yenye urefu wa kilomita 1.8, jengo la Kikosi cha Zimamoto na Uokoaji, sehemu ya maegesho ya ndege na magari pamoja na kioski. 

Kukamilika kwa uwanja huo kunatarajiwa kuongeza idadi ya watalii, kukuza mapato kwa Taifa na kuchochea shughuli za kiuchumi kwa jamii inayozunguka hifadhi.

Akikagua mradi huo jana Septemba 17, 2026, Kamishna wa Uhifadhi, Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) Massana Mwishawa amemwelekeza mkandarasi “China Henan International Cooperation, Group Co. LTD (CHICO)” kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati na kwa viwango vilivyokusudiwa ili kuleta tija kwa Taifa na jamii. Aidha, ameitaka Menejimenti ya Hifadhi kusimamia miradi hiyo kwa ufanisi sambamba na kuimarisha utekelezaji wa shughuli za uhifadhi na utalii.

Pia, Kamishna Mwishawa alifanya ukaguzi wa ujenzi wa barabara inayotokea lango la Kikoboga hadi lango la Chamgore yenye urefu wa kilometa 38, ambayo ukarabati wake umefikia asilimia 80. Ujenzi wa barabara hiyo unatekelezwa chini ya ufadhili wa fedha za Mfuko wa Kukuza Utalii nchini (TDL) unaosimamiwa na Wizara ya Maliasili na Utalii na kutekelezwa na TANAPA.

Barabara hiyo itaunganisha Lango la Chamgore lililopo upande wa Kilosa linalotarajiwa kuanza kujengwa mwaka huu, hivyo itaongeza wigo mkubwa wa mtandao wa njia za utalii ndani ya hifadhi kwa kuwawezesha watalii watakokuwa wanashuka na treni ya mwendo kazi (SGR) mjini Kilosa na kuingia hifadhini.

Hifadhi ya Taifa Mikumi ni miongoni mwa hifadhi zinazovutia katika ukanda wa mashariki mwa Tanzania, ikifahamika kwa urahisi wa kufikika na fursa ya kuona wanyamapori kwa haraka. Miongoni mwa vivutio vyake ni pamoja na makundi ya tembo, nyati, simba na twiga, pamoja na mandhari ya kuvutia na fursa nzuri ya kufanya utalii wa ndege.










Na Mwandishi Wetu

KAMPUNI ya Oryx Gas imekabidhi mitungi ya gesi 600 na vifaa vyake kwa wananchi wa Wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kampuni hiyo kuhakikisha Watanzania wengi zaidi wanapata fursa ya kutumia nishati safi, salama na rafiki kwa mazingira.

Oryx Gas imetoa mitungi hiyo ya gesi kwa wananchi hao kwa kushirikiana na Mbunge wa Jimbo la Namtumbo mkoani Ruvuma ambaye pia ni Waziri wa Katiba na Sheria Juma Homera kwa lengo la kuendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi nchini ili kulinda mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Oryx Gas Tanzania Iman Mtafya,Meneja Fedha wa kampuni hiyo Ashery Mbasha amesema kupitia Uwezeshaji huo Oryx Gas inaendelea kuunga mkono juhudi za Serikali za kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.

“Wilaya ya Namtumbo, kama ilivyo kwa maeneo mengi nchini Tanzania, imekuwa ikikabiliwa na changamoto ya matumizi makubwa ya kuni na mkaa. Hali hii imechangia kwa kiasi kikubwa ukataji wa miti na uharibifu wa mazingira.

“Hivyo kamahatua madhubuti hazitachukuliwa, vizazi vijavyo vinaweza kukumbana na uhaba mkubwa wa rasilimali za misitu na athari za mabadiliko ya tabianchi,”amesema na kuongeza kwa kutambua changamoto hiyo, Oryx Gas imeamua kuwa sehemu ya suluhisho kwa kuhamasisha matumizi ya gesi ya LPG kama mbadala wa kuni na mkaa.

Amesisitiza matumizi ya gesi ya kupikia yatasaidia kupunguza kasi ya ukataji miti, kuboresha afya za wananchi kwa kupunguza moshi majumbani, kuokoa muda wa kupika na kuongeza ubora wa maisha kwa ujumla.

Mbasha amesema dhamira ya Oryx Gas ni kuhakikisha Tanzania inafikia mabadiliko kamili ya matumizi ya nishati safi ya kupikia. Wilaya ya Namtumbo ni moja ya maeneo ambayo tumeyawekea kipaumbele katika safari hii muhimu.

“Oryx Gas pia imekuwa mshirika wa maendeleo katika wilaya hii ya Namtumbo kupitia miradi mbalimbali ya nishati safi. Miongoni mwa mafanikio hayo ni ufungaji wa mfumo wa hifadhi na usambazaji wa gesi ya LPG katika Shule ya Wasichana ya Samia Suluhu, hatua iliyowezesha taasisi hiyo kutumia nishati safi kwa manufaa ya wanafunzi na watumishi wake.”

Ametumia nafasi hiyo kutoa rai kwa wananchi wa Namtumbo hasa waliopata mitungi ya gesi ya Oryx kutumia majiko hayo kwa usalama na kuendelea kueneza elimu ya matumizi ya gesi ya LPG katika jamii zenu. Kwa pamoja tunaweza kujenga Namtumbo yenye mazingira bora, afya bora na maendeleo endelevu.

Awali akizungumza kwenye hafla hiyo Mbunge wa Jimbo la Namtumbo ,ambaye pia ni waziri wa Katiba na sheria Dk.Juma Homera ameishukuru kampuni ya Oryx kwa kuwapatia majiko 600 na Kati hayo majiko 215 yamekabidhiwa kwa wananchi wa Namtumbo na mengine yatapelekwa na kugawanywa kila kata kwa wananchi wa Wilaya hiyo.

Dk.Homera amesema Rais Dk.Samia Suluhu Hassan ambaye ni kinara wa nishati safi ya kupikia amekuwa akisisitiza utumiaji wa nishati safi hivyo amewataka wananchi kuunga mkono jitihada hizo za Rais na Serikali ya Awamu ya Sita kwa vitendo huku akiipongeza Oryx gas kwa ushirikiano ambao wamekuwa wakiutoa kwa wananchi wa Namtumbo.

Kwa upande wake Mama Lishe Anifa Mahela amepongeza mpango huo mzuri wa kutoa elimu na kugawa bure mitungi kwa wajasiriamali huku akiiomba Serikali na wadau kama Oryx kuwasaidia kupata mitungi ya gesi na majiko ya nishati safi kwa bei ya ruzuku kutokana na mtaji mdogo walionao.








-TAWA yaendelea kugusa maisha ya jamii


 Na. Beatus Maganja

UHIFADHI wa wanyamapori unapozalisha manufaa yanayoonekana katika maisha ya jamii wananchi hupata sababu zaidi ya kuona maeneo ya hifadhi kama sehemu ya maendeleo yao. Ni katika muktadha huo, Septemba 17, 2026, TAWA kupitia Pori la Akiba Mkungunero, ilipokabidhi vifaa vya elimu, michezo na ujenzi katika shule za Kwadelo B na Itaswi wilayani Kondoa.

Katika hatua hiyo, TAWA ilikabidhi mifuko 60 ya saruji, madaftari 190, jozi 15 za jezi na mipira miwili ikiwa ni sehemu ya urejeshaji wa faida zitokanazo na uhifadhi unaojenga daraja muhimu kati ya taasisi ya uhifadhi na jamii zinazoishi jirani na maeneo yenye rasilimali za wanyamapori.

Uhusiano huo ni muhimu kwa sababu mafanikio ya uhifadhi hayawezi kupimwa kwa idadi ya wanyamapori wanaolindwa peke yake, bali yanahusisha pia kiwango ambacho jamii zinazozunguka hifadhi zinaelewa, zinashiriki na kuona thamani ya kulinda rasilimali hizo.

Darasa lenye mazingira bora, mwanafunzi mwenye daftari au kijana anayeshiriki michezo anaweza kuwa mwanzo wa kujenga kizazi kinachoutazama uhifadhi kama sehemu ya ustawi wake.

Mifuko 60 ya saruji iliyotolewa ina umuhimu mwingine wa kimkakati. Mbali na kusaidia kuboresha na kuimarisha miundombinu ya shule, msaada huo umehusishwa na hatua za kujiandaa dhidi ya athari zinazoweza kusababishwa na mvua kubwa kufuatia tahadhari kuhusu uwezekano wa El Nino.

Kwa upande mwingine, madaftari, jezi na mipira vinagusa moja kwa moja maendeleo ya wanafunzi. Elimu hujenga maarifa, huku michezo ikichochea afya, nidhamu, ushirikiano na vipaji. Hivyo, kuwekeza katika maeneo haya kunapanua maana ya uhifadhi kutoka kulinda wanyamapori na kuifanya ihusishe pia ustawi wa watu wanaoishi kandokando ya maeneo yaliyohifadhiwa.

Ndiyo maana ujumbe wa Afisa Ujirani Mwema wa Pori la Akiba Mkungunero CII Tumaini Minja kwa wanafunzi hao kuhusu kusoma kwa bidii, kutunza vifaa walivyopatiwa na kuwa mabalozi wa uhifadhi una maana kubwa kwakuwa unalenga kujenga uelewa kwamba mwanafunzi wa leo anaweza kuwa mdau muhimu wa uhifadhi kesho hasa anapoanza mapema kuelewa uhusiano uliopo kati ya mazingira, wanyamapori na maendeleo ya jamii yake.

Mwitikio wa viongozi wa Shule ya Msingi Kwadelo B, Shule ya Sekondari Itaswi na Kijiji cha Itaswi nao unaonesha upande mwingine muhimu wa ushirikiano huu. Ahadi yao ya kuendelea kushirikiana na TAWA inaashiria kwamba ujirani mwema unapokuwa na manufaa yanayoonekana, unaweza kusaidia kujenga mazingira bora zaidi ya ushirikiano kati ya taasisi ya uhifadhi na wananchi.

Hatimaye, tukio la Kondoa linabeba ujumbe mkubwa kuliko thamani ya vifaa vilivyokabidhiwa. Linaonesha kuwa uhifadhi endelevu huimarika zaidi pale jamii inapokuwa sehemu ya manufaa yake.









Top News