Na Said Mwishehe,Michuzi TV

SHIRIKA la Umeme Tanzania (TANESCO) Mkoa wa Ubungo jijini Dar es Salaam limeendelea na operesheni yake maalum ya kuwabaini na kuwachukulia hatua wateja ambao wanatumia umeme bila kulipia wakiwa wameunganishiwa umeme na vishoka mtaani kinyume na utaratibu.

Katika operesheni hiyo TANESCO Mkoa wa Ubungo imekamata baadhi ya wateja wake katika maeneo ya Mabibo External,Mburahati na Kimara Kilungure na miongoni mwa wateja hao wamekuwa wakitumia umeme wa TANESCO bila kulipia kwa zaidi ya mwaka mmoja sasa.

Akizungumza leo Septemba 2,2026 wakati wa operesheni hiyo fundi wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Mkoa wa Ubungo Salum Bure amesema wamewakamata wateja ambao wamechepusha umeme kupitia vishoka.

“Katika eneo la Mtaa wa Amani uliopo Mabibo External kuna mteja tumekuta amechepusha umeme na mara ya mwisho amenunua umeme Agosti mwaka 2025.Hivyo kwa zaidi ya mwaka mmoja halipi umeme na ameunganishiwa na kishoka.

“Pia katika Mtaa wa Tanzanite uliopo Kimara Kirungule kuna mteja amekuwa akiliibia Shirika letu kwa kutumia umeme ambao haulipii na yeye amechepusha umeme kupitia vishoka,”amesema na kuongeza wateja wote ambao watabainika wameunganisha umeme kinyume na utaratibu hatua za kisheria zitachukuliwa

Bure amesema operesheni inayoendelea sasa inatokana na maelekezo ya Mkurugenzi wa Shirika hilo la TANESCO huku akitumia nafasi hiyo kuwataka wale wote wenye tabia ya kutumia umeme bila kuulipia waaache na wale wenye changamoto wafike katika ofisi zao kutoa taarifa.

Pia amewaomba wananchi wanapobaini baadhi yao kwa wamejiunganishia Umeme kinyume na utaratibu kwa kutumia vishoka kutoa Taarifa TANESCO kupitia namba ambayo unapiga bure ambayo ni 180

Kwa upande wake Mjumbe wa shina namba 10 katika Mtaa wa Amani eneo la Mabibo External Rose Peter amesema TANESCO wamefika katika eneo lake kukagua wale ambao wanaiba umeme kwa kujiunganishia bila utaratibu na kweli wamemkamata watu waliojiunganishia umeme bila utaratibu.

“Kwahiyo kwa wananchi wenzangu nitoe rai tuache tabia ya kuiibia TANESCO umeme .Hii iwe onyo kwa wote ambao wanaiba umeme na ushauri wangu tutumie mita zetu vizuri.”








Na MWANDISHI WETU


Shri Guru Singh Sabha – Jumuiya ya Sikh Dar es Salaam imekabidhi vifaa 100 vya kuhifadhia taka kwa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam ikiwa ni sehemu ya mchango wake katika kuunga mkono juhudi za Serikali za kuimarisha usafi na utunzaji wa mazingira jijini.

Akipokea vifaa hivyo , jijini Dar es Salaam, Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, ameishukuru Shri Guru Singh Sabha – Jumuiya ya Sikh Dar es Salaam kwa kuendelea kuunga mkono jitihada za Serikali, hususan maono ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan katika kusimamia usafi na utunzaji wa mazingira.

Mpogolo amesema Serikali inatambua na kuthamini mchango unaotolewa na Jumuiya ya Sikh katika kusaidia huduma mbalimbali za kijamii, kwani mbali na msaada huo, jumuiya hiyo imekuwa ikiandaa kambi mbalimbali za matibabu na vipimo bila malipo.

“Msaada huu ni chachu katika kutekeleza azma ya Rais Dk. Samia ya kulifanya Jiji letu la Dar es Salaam kuwa jiji lenye ushindani katika usafi barani Afrika na kuhakikisha linashika nafasi ya juu,” amesema Mpogolo.

Amesema Serikali wilayani humo itaendelea kusimamia utekelezaji wa azma hiyo na kuzitaka jamii, taasisi, mashirika na wadau mbalimbali kushiriki kikamilifu katika kusimamia usafi na utunzaji wa mazingira.

Awali, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, Elihuruma Mabelya, amesema mchango huo utaongeza nguvu katika usimamizi wa usafi na mazingira.

“Mwelekeo wa usafishaji wa maeneo yetu hautegemei Halmashauri peke yake. Tunategemeana kati ya Halmashauri na wadau kama Shri Guru Singh Sabha – Jumuiya ya Sikh Dar es Salaam. Tutaendelea kusimamia ushirikiano huu katika kuboresha usafi wa mazingira,” amesema Mabelya.

Shri Guru Singh Sabha – Jumuiya ya Sikh Dar es Salaam pia imeeleza kuthamini ushirikiano mkubwa ambao imekuwa ikiupata kutoka kwa Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, pamoja na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, Elihuruma Mabelya.

.Viongozi hao wamekuwa mstari wa mbele kutoa ushirikiano kwa taasisi na jumuiya mbalimbali za kidini, wakitambua kuwa taasisi za dini zina nafasi na wajibu muhimu katika kusaidia kujenga jamii yenye maadili mema, umoja, kuheshimiana, uwajibikaji na mshikamano.

Ushirikiano huo kati ya Serikali na taasisi za kidini unatoa nafasi kwa jumuiya mbalimbali kushiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii na maendeleo, kwa lengo la kujenga jamii bora na yenye maadili kwa manufaa ya wananchi wote.

Mwakilishi wa Shri Guru Singh Sabha – Jumuiya ya Sikh Dar es Salaam, Jasdeep Singh Babhra, amesema mazingira si wajibu wa Serikali pekee bali ni jukumu la jamii nzima, hivyo Jumuiya ya Sikh imeona umuhimu wa kuunga mkono jitihada kubwa za Serikali chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, ambaye amekuwa mstari wa mbele katika kuhimiza utunzaji wa mazingira.

Babhra, amesema Shri Guru Singh Sabha – Jumuiya ya Sikh Dar es Salaam imekabidhi vifaa 100 vya kuhifadhia taka na itaendelea kushirikiana na Serikali katika shughuli mbalimbali za kijamii na maendeleo.

Amesema Jiji la Dar es Salaam linaendelea kukua na kuwa na ongezeko kubwa la watu, hivyo usafi na utunzaji wa mazingira unahitaji ushirikiano wa pamoja kati ya Serikali, taasisi, jumuiya za kidini, sekta binafsi na wananchi.

Diwani wa Kata ya Gerezani, Fatuma Abubakar, amesema Shri Guru Singh Sabha – Jumuiya ya Sikh Dar es Salaam imekuwa mstari wa mbele kushirikiana na Serikali katika kusaidia jamii, hivyo akaishukuru kwa msaada huo wa vifaa muhimu vya usafi.

Shri Guru Singh Sabha – Jumuiya ya Sikh Dar es Salaam imesisitiza kuwa itaendelea kushirikiana na Serikali katika mipango inayolenga kuboresha mazingira, afya, ustawi wa jamii na kujenga jamii yenye maadili, mshikamano na uwajibikaji.






Na Janeth Raphael -MichuziTv -Bungeni Dodoma 

SERIKALI imesema imekamilisha mapitio ya Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Vijana ya Mwaka 2007 na kwamba Toleo la Mwaka 2024 tayari linaendelea kutekelezwa nchini.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Zainab Katiba, kwa niaba ya Waziri wa Maendeleo ya Vijana, wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Timida Mpoki Fyandamo, aliyetaka kujua ni lini Serikali itapitia upya Sera ya Maendeleo ya Vijana ya Mwaka 2007.

Naibu Waziri amesema kabla ya kufanya mapitio hayo, Serikali ilifanya tathmini ya utekelezaji wa sera hiyo mwaka 2022 kwa lengo la kubaini mafanikio yaliyopatikana, changamoto, mapungufu pamoja na masuala mapya yaliyojitokeza katika maendeleo ya vijana.

Amesema matokeo ya tathmini hiyo, pamoja na maoni ya wadau mbalimbali, yalitumika katika kuandaa Toleo la Mwaka 2024 la Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Vijana.

Kwa mujibu wa Serikali, sera hiyo iliidhinishwa na Baraza la Mawaziri Aprili 25, 2024 na kuzinduliwa rasmi jijini Dodoma Agosti 12, 2024.

Amesisitiza kuwa Serikali kwa sasa haipo katika hatua ya kupanga kufanya mapitio ya sera hiyo, kwa kuwa zoezi hilo tayari limekamilika na Toleo la Mwaka 2024 linaendelea kutekelezwa.

Aidha, Serikali imeandaa Mkakati wa Utekelezaji wa Sera hiyo kwa kipindi cha mwaka 2024 hadi 2034, unaoainisha afua zitakazotekelezwa, matokeo yanayotarajiwa, viashiria vya utekelezaji, muda wa utekelezaji pamoja na majukumu ya wadau mbalimbali.

Serikali imesema itaendelea kuratibu, kufuatilia na kutathmini utekelezaji wa sera hiyo ili kuhakikisha changamoto na mahitaji ya vijana yanabainika na kushughulikiwa kwa wakati.



Na Janeth Raphael - MichuziTv


Watanzania kutoka makundi mbalimbali wanatarajiwa kukutana Novemba 7 mwaka huu katika Tanzania National Prayer Breakfast (TNB), jukwaa linalolenga kuliombea taifa, kuimarisha umoja na mshikamano pamoja na kujadili masuala yanayohusu uongozi, maadili, utumishi wa umma na maendeleo ya nchi.

Tanzania National Prayer Breakfast inalenga kuwaunganisha Watanzania bila kujali tofauti zao za kidini, kisiasa au kijamii, kwa kuwapa nafasi viongozi, vijana, wanawake na makundi mbalimbali kukutana, kuombea taifa na kujadili namna ya kujenga Tanzania yenye maadili, umoja na watu wanaoshirikiana.

Mwenyekiti wa Tanzania National Prayer Breakfast, Waziri Mkuu mstaafu Frederick Sumaye, amesema jukwaa hilo ni muhimu katika kuwaunganisha Watanzania na kutoa nafasi kwa viongozi wa kitaifa kuzungumza kuhusu masuala mbalimbali yanayolihusu taifa, akisisitiza kuwa umoja wa kitaifa ni wajibu wa kila Mtanzania na unapaswa kukumbushwa mara kwa mara.

“Lengo letu ni kuendelea pamoja, taifa moja na watu wamoja. Ni wajibu wetu kukumbushana kama taifa umuhimu wa kuwa kitu kimoja,” amesema Sumaye.

Amesema mwaka huu wamekusudia kufanya tukio hilo kwa kiwango kikubwa zaidi ili Watanzania wengi watambue umuhimu wa jukwaa hilo na Serikali pamoja na Bunge kulitambua kama sehemu muhimu ya kuimarisha umoja, maadili na mshikamano wa taifa.

Kwa mujibu wa Sumaye, Tanzania National Prayer Breakfast si jukwaa la dini moja wala kundi fulani, bali linawakutanisha watu wa dini mbalimbali, vyama mbalimbali na makundi tofauti kwa lengo la kuliombea taifa na kujenga misingi ya kuendelea kuwa taifa moja lenye watu wanaoshirikiana na kuheshimiana.

Amesema maandalizi ya tukio hilo yataanza Novemba 5 kwa semina, huku Novemba 6 kukiwa na mjumuiko maalumu wa wanawake, ambao amesema wamekuwa wakibaki nyuma katika kushiriki katika majukwaa ya aina hiyo. Vijana nao watapewa nafasi katika programu hiyo kutokana na umuhimu wao katika ujenzi wa taifa, huku wakilenga kuwajenga katika maadili, uongozi bora na uwajibikaji.

Amesema kilele cha shughuli hizo kitakuwa Novemba 7, siku ambayo itafanyika Tanzania National Prayer Breakfast na ambapo wanatarajia mgeni rasmi kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Pia wanatarajia kushiriki wageni kutoka mataifa mbalimbali, wakiwamo wawakilishi wa mabunge, mahakama, mashirika ya kimataifa, vijana na wanawake kutoka maeneo ya mijini na vijijini.

Sumaye amesema ushiriki wa watu kutoka ndani na nje ya Tanzania unaonyesha kuwa Tanzania National Prayer Breakfast ni programu yenye mtazamo mpana inayolenga kuunganisha watu kupitia uongozi wa maadili, maombi na ushirikiano. Amesema jukwaa hilo linashirikisha wadau mbalimbali wakiwamo KLNT, Kingdom Leadership, Tanzania World Vision pamoja na kikundi cha waombaji wa wabunge, ambao wamekuwa sehemu ya maandalizi ya tukio hilo.

Aidha, amesema wanataka Tanzania National Prayer Breakfast iwe sehemu inayotambulika zaidi kitaifa na kuendelea kutumika kama jukwaa la kuimarisha umoja na mshikamano wa taifa, huku wakitarajia Serikali na Bunge kuona umuhimu wa kulibeba na kuliendeleza katika miaka ijayo. Amesema iwapo Bunge litaridhia, mwakani wanataka suala hilo lipewe nafasi kubwa zaidi kwa sababu jambo linalolenga kuwaunganisha Watanzania halipaswi kuishia njiani wala kukosa kuendelezwa.

Kwa upande wake, Katibu wa Tanzania National Prayer Breakfast, L. Isack Mpatwa, amesema jambo la msingi ni kuhakikisha kunakuwa na mkakati madhubuti wa kuwakutanisha watu kutoka makundi mbalimbali ili kujenga umoja na mshikamano wa kitaifa.

Mpatwa amesema jukwaa hilo linapaswa kuendelea kuwa eneo la kukumbushana kuhusu maadili, uongozi bora na wajibu wa kila mmoja katika kulijenga taifa, akisisitiza kuwa lengo si kwa kundi moja pekee bali dini zote na vyama vyote vinapaswa kuwa sehemu ya juhudi hizo kwa kuwa Tanzania ni ya watu wote.

Amesema Tanzania National Prayer Breakfast ni sehemu ya programu pana ya uongozi wa maadili, utumishi wa umma na maombi jumuishi inayolenga kuwaunganisha viongozi na wananchi katika kujenga taifa lenye umoja na mshikamano.

Kwa mujibu wa Mpatwa, kupitia mikutano hiyo Watanzania wanapata nafasi ya kukutana, kuombea nchi yao na kukumbushana umuhimu wa kuendelea kushirikiana katika kulinda umoja na amani ya taifa, huku Tanzania National Prayer Breakfast ikiendelea kulenga kuwa jukwaa linalowakutanisha Watanzania wa makundi mbalimbali katika kujenga taifa lenye maadili, mshikamano na mwelekeo wa pamoja.





Na Mwandishi Wetu


SERIKALI imeandaa Mpango wa Taifa wa Dharura wa Kukabiliana na Madhara ya El Niño, huku ikiwataka wananchi kuchukua tahadhari mapema dhidi ya athari zinazoweza kujitokeza kutokana na mvua kubwa zinazotarajiwa katika msimu wa Vuli 2026/27.

Taarifa hiyo imetolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Prof. Palamagamba Kabudi, wakati akitoa taarifa kwa vyombo vya habari kuhusu utekelezaji wa mpango huo.

Mpango huo umeandaliwa kufuatia utabiri uliotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) Agosti 18, 2026, uliotabiri uwepo wa hali ya El Niño yenye nguvu katika msimu wa Vuli 2026/27.

Kwa mujibu wa Serikali, mpango huo unalenga kuimarisha utayari na kuhakikisha hatua za mapema zinachukuliwa katika kuzuia, kujiandaa, kukabili na kurejesha hali ya kawaida baada ya kutokea kwa madhara yanayoweza kusababishwa na El Niño.

Miongoni mwa hatua zilizopangwa ni kukarabati na kuboresha miundombinu inayoweza kuathiriwa na mvua kubwa, ikiwemo barabara, madaraja, mitaro na reli, pamoja na kuhakikisha huduma muhimu za afya, elimu, maji, umeme na mawasiliano zinaendelea kupatikana katika maeneo hatarishi.

Aidha, Serikali imepanga kuimarisha akiba ya chakula, vifaa vya uokoaji na misaada ya kibinadamu, pamoja na kuandaa maeneo ya muda kwa ajili ya kuwahifadhi wananchi watakaoweza kuathiriwa na maafa.

Serikali imeeleza kuwa makadirio ya rasilimali zinazohitajika kutekeleza mpango huo kwa sekta zote yanafikia takribani Sh bilioni 730, wakati fedha zilizotengwa katika bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2026/27 kwa ajili ya shughuli hizo ni Sh bilioni 10.

Pamoja na maandalizi hayo, Serikali imewataka wananchi kutotumia mvua hizo kwa hofu pekee, bali pia kuzitumia kama fursa kwa shughuli za uzalishaji, ikiwemo kilimo, ufugaji, uvunaji wa maji na uvuvi.

Wananchi wametakiwa kutumia mbinu bora za kilimo, kuchagua mazao na mbegu zinazofaa kwa msimu wa Vuli, huku wakichukua tahadhari dhidi ya maeneo yanayoweza kukumbwa na mafuriko, maporomoko ya ardhi na milipuko ya magonjwa.

Serikali pia imewataka wananchi kufuatilia kwa karibu taarifa rasmi za hali ya hewa zinazotolewa na TMA, kuondoka mapema katika maeneo hatarishi na kutoa taarifa kwa mamlaka husika mara maafa yanapotokea.

Ofisi ya Waziri Mkuu imeeleza kuwa Agosti 26, 2026 ilitoa maelekezo kwa Wakuu wa Mikoa inayoweza kuathiriwa na mvua za El Niño kuhakikisha maandalizi yanafanyika mapema ili kupunguza madhara yanayoweza kujitokeza.

Serikali imesisitiza kuwa ushirikiano kati ya Serikali, mamlaka za mikoa na halmashauri pamoja na wananchi ni muhimu katika kuhakikisha athari za El Niño zinadhibitiwa na fursa zinazotokana na mvua hizo zinatumika kwa shughuli za maendeleo.





Na Belinda Joseph – Dodoma

Chama cha Walimu Tanzania (CWT) kimesema kinaendelea kuimarisha huduma za utetezi kwa wanachama wake, ikiwemo kuwapatia msaada walimu wanachama wanaokabiliwa na changamoto mbalimbali za kikazi na kisheria.

Hayo yameelezwa na Kaimu Katibu Mkuu wa CWT, Protas Magesa, Septemba 2, 2026, jijini Dodoma, wakati wa kikao cha viongozi wa Chama cha Walimu Tanzania na walimu wanachama mahali pa kazi kutoka Ofisi ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, akieleza kuwa chama hicho kinatumia fedha nyingi kuhakikisha walimu wanapata huduma ya utetezi inapohitajika.

Magesa amesema CWT pia inaendelea kutekeleza miradi mbalimbali inayolenga kuwajengea uwezo walimu, ikiwemo kutoa elimu kwa walimu wenye mahitaji maalum kuhusu matumizi ya mifumo, na mwendelezo wa utekelezaji wa miradi mingine huku akisisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya chama hicho na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ili kubaini maeneo ambayo wanaweza kushirikiana katika kuwahudumia na kutatua changamoto zinazowakabili walimu.

Aidha, amesema CWT kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali imeandaa programu ya kutoa elimu kwa walimu wa sayansi ambao ni wanachama wa chama hicho kuhusu matumizi salama ya kemikali wanazotumia katika utekelezaji wa majukumu yao, amesema utoaji wa elimu hiyo unatarajiwa kuanza mwezi Oktoba mwaka huu katika Mkoa wa Mara na baadae kuendelea katika maeneo mengine nchini.

Akizungumza Afisa kutoka ofisi ya Kamishna wa Elimu Mwalimu Mbutorwe Mwakyima, amesema ushirikiano kati ya CWT na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ni muhimu katika kusikiliza na kutatua changamoto zinazowakabili walimu, amesema wanapopata haki zao na mazingira bora ya kutekeleza majukumu yao, wanaweza kufanya kazi kwa ufanisi zaidi na hivyo kuchangia katika kuboresha sekta ya elimu nchini.

Kwa upande wake, Afisa udhibiti ubora wa shule kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Bartolomeo Mwekila, amesema CWT imekuwa na mchango katika kuwasaidia walimu katika masuala mbalimbali, ikiwemo upandishaji wa madaraja, aidha ameshauri chama hicho kuendelea kuwawezesha walimu kupitia mafunzo ya mara kwa mara pamoja na kuwatafutia fursa za ajira ndani na nje ya nchi, andapo nafasi zitahitajika.






Na Mwandishi Wetu.

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imekutana na kufanya mazungumzo na watangazaji na waandaaji wa kipindi cha Good Morning kinachorushwa na Wasafi FM, ambapo imewakumbusha umuhimu wa kuzingatia sheria, kanuni na maadili ya uandishi wa habari katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Kikao hicho kimefanyika leo, Septemba 2, 2026, katika Makao Makuu ya JAB, Mtaa wa Jamhuri, jijini Dar es Salaam, kikilenga kuimarisha uelewa wa watangazaji hao kuhusu misingi ya weledi, uwajibikaji na matumizi sahihi ya majukwaa ya habari.

Akizungumza katika kikao hicho, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, amefafanua matakwa ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229; Sheria ya Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta, Sura ya 306; pamoja na kanuni zake zinazopaswa kuzingatiwa katika utayarishaji na utangazaji wa maudhui.

Wakili Kipangula ameeleza kuwa kuzingatia sheria na maadili ni msingi wa kulinda heshima ya taaluma, haki za watu wanaohusika katika maudhui na imani ya jamii kwa Waandishi wa Habari.

Baada ya mazungumzo hayo, watangazaji wakongwe Gelard Hando na Hilary Mtuta, maarufu kama Zembwela, walikabidhiwa vitambulisho vyao vya ithibati ya uandishi wa habari baada ya kukidhi vigezo vilivyowekwa kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari.

Makabidhiano hayo yamekamilisha hatua ya kuwatambulisha rasmi kama Waandishi wa Habari wenye ithibati, wenye wajibu wa kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi, maadili na uwajibikaji. 




Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, akizindua Programu ya Mining for a Brighter Tomorrow (MBT) katika eneo la Nyamongo, mkoani Mara, inayolenga kupanua fursa za maeneo ya uchimbaji, taarifa za kijiolojia na leseni kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu.

Helikopta ikifanya utafiti wa madini kwa njia ya anga katika eneo la Nyamongo ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Programu ya MBT, hatua itakayosaidia kupata taarifa za kijiolojia kwa ajili ya utafiti wa kina na uchorongaji katika maeneo yaliyotengwa kwa wachimbaji wadogo.



Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, amekutana na ujumbe wa kampuni ya madini ya AngloGold Ashanti kujadili maendeleo ya shughuli za kampuni hiyo na namna ya kuimarisha uhusiano wake na Tanzania.

Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, alifanya mazungumzo hayo Jumanne, Septemba 1, 2026, wakati ujumbe wa AngloGold Ashanti ulipomtembelea ofisini kwake jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kumweleza maendeleo ya shughuli za kampuni hiyo na maslahi yake ya kibiashara nchini Tanzania.

Ujumbe huo uliongozwa na Bi. Lizelle Marwick, Afisa Mkuu wa Sheria wa AngloGold Ashanti, na ulijumuisha Balozi Baso Sangqu, Makamu wa Rais Mwandamizi anayeshughulikia Uendelevu wa AngloGold Ashanti, pamoja na Bw. Simon Shayo, Makamu wa Rais anayeshughulikia Uendelevu na Ushirikishwaji wa wadau wa Geita Gold Mining Limited (GGML).

AngloGold Ashanti ni mojawapo ya kampuni kubwa duniani katika sekta ya madini na inafanya shughuli zake nchini kupitia kampuni tanzu ya GGML.

Akizungumza na ujumbe huo, Bw. Mchechu alisema OTR, kama mwakilishi wa Serikali katika umiliki wa hisa, ni mshirika mwenza wa kampuni hiyo, akisisitiza kuwa mafanikio ya biashara yana manufaa kwa pande zote mbili.

“Nyie msipopata matokeo, na sisi hatupati matokeo; na nyie mkipata matokeo, na sisi tunapata matokeo,” alisema.

Alisema OTR inafanya kazi kwa karibu na mamlaka husika, huku taasisi hizo zikiwa na mtazamo mmoja kuhusu masuala muhimu ili kutengeneza mazingira rafiki zaidi ya uwekezaji.

Bw. Mchechu alisema OTR inalenga kujenga uhusiano wa muda mrefu na AngloGold Ashanti unaozingatia uelewano, utawala bora wa kampuni na mafanikio endelevu ya biashara.

Alisisitiza pia umuhimu wa kuwa na bodi za wakurugenzi zenye watu wenye uwezo, uelewa wa biashara na mtazamo wa kimkakati, akibainisha kuwa wajumbe wa bodi wanapaswa kuwa na uwezo wa kuongeza thamani katika uendeshaji na mwelekeo wa kampuni, hususan katika taasisi zinazochangia kodi na gawio kwa Serikali.

Kwa upande wake, Bi. Marwick alisema AngloGold Ashanti inathamini uhusiano wake na Serikali za nchi ambako inafanya shughuli zake, huku akieleza kuwa kampuni hiyo inatambua umuhimu wa uhusiano wake wa muda mrefu na Serikali ya Tanzania.

Alisema kampuni hiyo inalenga kujenga ushirikiano wa kweli unaowezesha kila upande kutumia uwezo na uzoefu wake katika kutengeneza matokeo yenye manufaa kwa kampuni na nchi kwa ujumla.

Katika kuimarisha uelewa na uwezo wa wajumbe wa bodi, Bi. Marwick alisema AngloGold Ashanti iko tayari kushirikiana katika programu za mafunzo na utangulizi wa majukumu ya bodi, zitakazohusu wajibu wa wajumbe, taratibu za uendeshaji wa bodi na uelewa wa masuala ya fedha.

Pia alipendekeza wajumbe wa bodi kufanya ziara katika Mgodi wa Dhahabu wa Geita ili kupata uelewa wa moja kwa moja kuhusu shughuli za uchimbaji, pamoja na masuala ya kitaalamu yanayohusu rasilimali na akiba ya madini.

Alisema uhusiano mzuri uliopo kati ya kampuni hiyo na Serikali unaweza kuwa msingi muhimu wa kuendeleza shughuli zake katika maeneo mengine yenye leseni za utafiti nchini, kwa kuwa kampuni inaweza kupanua shughuli zake kwa urahisi zaidi katika mazingira ambayo tayari ina shughuli, miundombinu na uhusiano mzuri wa kikazi na Serikali.





Top News