Na Benny Mwaipaja, Congo, Brazaville.

Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amewasili nchini Congo, Brazzaville, amabako atashiriki Mkutano Mkuu wa 61 wa mwaka 2026 wa Bodi ya Magavana wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB) na Mkutano Mkuu wa 52 wa Mwaka wa Mfuko wa Maendeleo wa Benki hiyo (ADF), uliopangwa kufanyika kuanzia tarehe 25 hadi 29 mwaka 2026, katika Mji Mkuu wa Congo, Brazaville.
Katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Brazaville, Maya Maya, Mheshimiwa Balozi Omar, alilakiwa na Balozi wa Tanzania nchini Congo, Brazaville, Mhe. Said Juma Mshana.

Katika msafara huo, Mhe. Balozi Omar, ambaye ni Gavana wa Benki ya Maendeleo ya Afrika, ameambatana na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mlipaji Mkuu wa Serikali ambaye pia katika Muundo wa Benki ya Maendeleo ya Afrika ni Gavana Mbadala wa Benki hiyo (Alternative Governor), Dkt. Natu El-maamry Mwamba na Naibu Katibu Mkuu ambaye pia ni Kamishna wa Fedha za Nje, Bw. Rished Bade.

Zaidi ya wajumbe 3,000 kutoka nchi mbalimbali za Afrika na Kimataifa, wanatarajiwa kuhudhuria Mkutano Mkuu huo, Utakaofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Kintélé, wakiwemo Marais na Wakuu wa Serikali za Afrika, Mawaziri wa Fedha, Magavana wa Mabenki Kuu, washirika wa maendeleo, wawakilishi wa sekta binafsi, viongozi wa asasi za kiraia, wasomi, taasisi za utafiti, NGOs, na wadau wengine.

Kauli mbiu ya mwaka huu ni: “Kuhamasisha Ufadhili wa Maendeleo ya Afrika kwa Wingi katika Dunia Iliyogawanyika”. Kauli hii inasisitiza umuhimu wa kuziba pengo la kifedha linalokua kwa mahitaji ya maendeleo ya Afrika, hasa katika mazingira ya kisiasa na kiuchumi duniani yanayobadilika kwa kasi.

Mkutano pia utajadili masuala mtambuka kama mageuzi ya kidijitali, uimarishaji wa taasisi na utawala bora. Haya yote yanalingana na utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs), Mkataba wa Paris wa Mabadiliko ya Tabianchi, Ajenda 2063 ya Umoja wa Afrika, na Mikakati Mikuu Mitano ya Benki ya Maendeleo ya Afrika (High 5s).











Na Janeth Raphael MichuziTv - Iringa

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mwigulu Nchemba, ameonyesha kutoridhishwa na baadhi ya hospitali nchini kuendelea kuwaagiza wananchi kununua dawa nje ya hospitali licha ya Serikali kutoa fedha kwa ajili ya ununuzi wa dawa hizo.

Dkt. Mwigulu amesema Serikali imekuwa ikipeleka fedha nyingi katika sekta ya afya ili kuhakikisha hospitali na vituo vya kutolea huduma za afya vinakuwa na dawa za kutosha kwa ajili ya wananchi, huku taarifa za vitabu zikionyesha kuwa kiwango cha upatikanaji wa dawa kinafikia zaidi ya asilimia 90.

Hata hivyo, amesema bado wananchi wengi wanapofika hospitalini kupata matibabu huambiwa kwenda kununua dawa katika maduka binafsi jambo alilolitaja kuwa ni “mambo ya ajabu” yasiyopaswa kuendelea kuvumiliwa.

“Mtu anaambiwa dawa zipo kwa mujibu wa taarifa na kumbukumbu za hospitali, lakini mgonjwa akifika anatakiwa kwenda kununua dawa mtaani. Haya ni mambo ya ajabu kabisa na hayakubaliki,” amesema Dkt. Mwigulu.

Kutokana na hali hiyo, Waziri Mkuu amesema tayari ametoa maelekezo kwa Mganga Mkuu pamoja na watendaji wa Mkoa wa Iringa kuhakikisha dawa zote zinazonunuliwa kwa fedha za Serikali zinawafikia wananchi kama ilivyokusudiwa.

Amesisitiza kuwa viongozi na watendaji wa sekta ya afya wanapaswa kusimamia kwa karibu matumizi ya fedha zinazotolewa na Serikali ili kuondoa changamoto zinazowakabili wananchi wanapohitaji huduma za matibabu.

“Natoa maelekezo kwa Mganga Mkuu pamoja na watendaji wote kuhakikisha dawa zitakazotumika katika hospitali zote za Mkoa wa Iringa zinasimamiwa ipasavyo. Mimi mambo ya ajabu ajabu sina ustaarabu nayo. Ninachotaka ni wananchi wanufaike na dawa zinazotolewa na Serikali,” alisisitiza.

Dkt. Mwigulu amesema Serikali ya Awamu ya Sita inaendelea kuboresha huduma za afya nchini kwa kuongeza bajeti ya dawa, vifaa tiba pamoja na miundombinu ya hospitali ili wananchi wapate huduma bora karibu na maeneo yao.

Aidha, amewataka watumishi wa sekta ya afya kufanya kazi kwa uadilifu na kuwahudumia wananchi kwa haki bila kuwapa usumbufu usio wa lazima, akisisitiza kuwa fedha zinazotolewa na Serikali zinapaswa kuonekana moja kwa moja katika huduma wanazopata wananchi.

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo wilayani Kilolo, mkoani Iringa, alipokuwa akizungumza na wananchi katika moja ya ziara yake ya kikazi mkoani humo, ambapo alipokea na kusikiliza changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi katika sekta mbalimballina huduma za kijamii.


Na Mwandishi Wetu, Michuzi TV

TANZANIA inatarajiwa kupokea ujumbe wa viongozi wa elimu ya juu kutoka Malaysia, wakiwemo maofisa kutoka Wizara ya Elimu ya Malaysia, Education Malaysia Global Services (EMGS) pamoja na wawakilishi wa vyuo vikuu tisa watakaoshiriki Maonesho ya Elimu ya Malaysia yatakayofanyika Juni 1–3, 2026 katika Hoteli ya Serena, Dar es Salaam.

Maonesho hayo yanayoratibiwa kwa ushirikiano wa Global Education Link (GEL) na wadau wa elimu kutoka Malaysia yanalenga kufungua fursa za udahili, ufadhili wa masomo, ushirikiano wa kitaaluma pamoja na kuimarisha mahusiano ya elimu kati ya Tanzania na Malaysia.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa Global Education Link, Abdumalik Mollel, alisema ujio huo ni wa kimkakati kwa kuwa unaleta pamoja mamlaka muhimu za elimu ya juu, vyuo vikuu na taasisi zinazoratibu wanafunzi wa kimataifa.

Alisema vyuo vitakavyoshiriki vitatoa taarifa kuhusu programu za masomo, gharama za elimu, mazingira ya kujifunzia, taratibu za udahili pamoja na nafasi za ufadhili wa masomo kwa wanafunzi wa Tanzania.

“Hii siyo maonesho ya kawaida ya udahili pekee. Ni fursa ya kuunganisha Tanzania na Malaysia katika elimu ya juu, scholarship, tafiti, ubunifu na ushirikiano wa kitaaluma,” alisema Mollel.

Miongoni mwa vyuo vinavyotarajiwa kushiriki ni Asia Pacific University of Technology and Innovation (APU), University of Malaya, University Putra Malaysia (UPM), University Kebangsaan Malaysia (UKM), UCSI University, University Kuala Lumpur, University Selangor (UNISEL) na Putra Business School.

Mollel alisema maonesho hayo pia yatafungua fursa za ushirikiano kati ya vyuo vya Tanzania na Malaysia kupitia makubaliano ya ushirikiano (MoU), tafiti za pamoja, ubadilishanaji wa wanafunzi na wahadhiri pamoja na programu za kitaaluma na ubunifu.

Alisema maonesho hayo yanatoa fursa muhimu kwa wanafunzi, wazazi, taasisi za elimu na Serikali katika kujenga mahusiano ya kimataifa na kuongeza nafasi za elimu kwa vijana wa Tanzania.


Katika mwendelezo wa kuimarisha utimamu wa mwili na akili, Benki ya CRDB imeendeleza programu yake ya Wellness Day inayolenga kuwapa wafanyakazi nafasi ya kujali afya zao kwa kuwa na uwiano kati ya majukumu ya kiofisi na maisha binafsi Jijini Bunjumbura - Burundi.

Kupitia Wellnes Day inayoadhimishwa tangu mwaka 2021, wafanyakazi wa Benki ya CRDB hupata mafunzo na semina juu ya siha ya mwili, lishe bora pamoja na ustawi wa akili.

Akizungumza katika programu hiyo ilyofanyika viwanja vya Serenity Garden (Avenue du Large) ambako wafanyakazi walikuwa wanafanya mazoezi ya aina tofauti pamoja na kushiriki michezo sambamba na kupima afya. Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Benki Burundi, Fredric Siwale mara baada ya kuwaongoza katika mazoezi ya viongo, alisema mfanyakazi anapokuwa na afya njema na saikolojia yake ikakaa sawa basi atakuwa na uwezo mkubwa wa kutimiza majukumu yake na kuwahudumia wateja kwa viwango vinavyokubalika.

“Wakati wote Benki yetu imekuwa mstari wa mbele katika kuwajali sana wateja na wadau wetu. Wakati wote tunalenga kuwapa huduma bora lakini tunafahamu hatuwezi kufanikisha hilo bila kuwa na wafanyakazi wenye utulivu wa mwili na akili, hii ndio maana ya kuwa Benki kiongozi ambapo kwa mwaka huu Benki imetunukiwa tuzo ya Mwajiri bora "Top Employer" aliongeza Siwale.

Wellness Day ni mkakati wa Benki yetu ya CRDB kutoa fursa kwa wafanyakazi kupima afya, kupata ushauri wa vyakula vya kutumia pamoja na utatuzi wa changamoto nyingine yoyote inayoweza kupunguza ufanisi wa mfanyakazi,” aliongeza Siwale.

Huu ni mwendelezo wa programu hiyo ambayo kwa mwaka huu ilizinduliwa jijini Mwanza, baadae kufanyika kanda ya Kasikazini, Kusini, Magharibi na sasa imefanyika Burundi lengo ni kuwafikia wafanyakazi wote katika kanda zote nane za Benki ya CRDB pamoja na nje ya nchi ambako benki inatoa huduma kuhakikisha wafanyakazi wote wa taasisi hii kubwa zaidi ya fedha nchini inakuwa na wafanyakazi wenye weledi na wanaotoa huduma za kiwango cha juu.

Akieleza jinsi walivyojipanga kufikisha programu hiyo kwa kila mfanyakazi, Kaimu Mkurugenzi Rasiliamali watu wa Benki ya CRDB, Timoth Fasha amesema wataalamu wa afya wanashauri juu ya kupata usingizi wa kutosha, kufanya mazoezi ya mwili, kupata lishe bora pamoja na ushauri juu ya afya ya akili hivyo ni muhimu kwa kila mfanyakazi kuyafahamu mambo haya na kuyaishi.

“Mfanyakazi anaweza akajisahau kuijali afya yake kutokana na sababu mbalimbali za majukumu ya kikazi. Hivo kupitia Programu ya Wellness Day, tunawakumbusha wafanyakazi wetu umuhimu wa kuwa na ratiba ya kuulinda mwili kwa vipimo vya kitabibu, mazoezi pamoja na ushauri wa kitaalamu. Hii ni muhimu kwa sababu mafanikio ya Benki ya CRDB yanatokana na mchango wa kila mmoja wetu hivyo ni muhimu kuwa na afya njema ili kuendeleza ubora huo kwa wateja wetu,” amesema Fasha.

Kutokana na wingi wa majukumu, mfanyakazi anaweza kujikuta anatumia muda mwingi kukaa ofisini hivyo kutofanya mazoezi ya mwili au kuzungumza na watu wengine hali ambayo ikidumu kwa muda mrefu inaweza kusababisha msongo wa mawazo iwapo kutatokea hata changamoto ndogo tu kwa mhusika.

Kupitia Wellness Day, wafanyakazi wa Benki ya CRDB wanapata fursa ya kushiriki michezo ya aina tofauti, mazoezi ya viungo pamoja na kukutana na madaktari na washauri nasaha wanaotoa elimu ya saikolojia, mahusiano, matibabu, msongo wa mawazo, pamoja na lishe na usimamizi wa mtindo wa maisha.




Benki ya NMB imesema itaendelea kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar pamoja na taasisi zake katika kuimarisha mifumo ya malipo, makusanyo, huduma za kidijitali na suluhisho za kifedha zinazolenga kuongeza ufanisi wa huduma kwa wananchi na wawekezaji.

Kauli hiyo imetolewa wakati wa Mkutano wa Watendaji Wakuu na Wenyeviti wa Bodi wa Taasisi za Kizanzibari unaofanyika Golden Tulip Airport Hotel, Zanzibar, kuanzia Mei 23 hadi 25, 2026, ambapo Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, aliwataka viongozi wa taasisi hizo kuleta mageuzi ya kiutendaji yatakayoongeza tija, kupunguza utegemezi kwa Serikali Kuu na kuwezesha taasisi kutoa gawio kwa Serikali.

Akifungua mkutano huo, Rais Dkt. Mwinyi alisema kasi ya maendeleo itaongezeka zaidi kupitia ushirikiano imara na sekta binafsi, akitolea mfano mabenki yanayofanya vizuri nchini kwa kuonyesha ukuaji mkubwa, faida nzuri na kutoa gawio kubwa kwa Serikali.

 “Taasisi zetu zinapaswa kujifunza kutoka kwenye mifano mizuri ya sekta binafsi, hasa mabenki binafsi yanayoonyesha ufanisi, faida na mchango mkubwa wa gawio kwa Serikali,” alisema Dkt. Mwinyi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Biashara za Serikali wa NMB, Bi. Vicky Bishubo, alisema NMB inaona Zanzibar kama mshirika muhimu katika ajenda ya maendeleo kupitia uwekezaji, uchumi wa bluu, utalii, biashara, teknolojia na huduma za kifedha. Alisema NMB tayari inashirikiana na EGAZ, ZIPA na taasisi nyingine za Zanzibar katika kuboresha huduma za kidijitali, uwekezaji na uhifadhi wa maeneo ya kimkakati, huku pia ikitoa mafunzo kwa zaidi ya wajasiriamali 10,000 wa Zanzibar wanaojihusisha na mwani, chumvi na uvuvi.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, akipokea zawadi maalum kutoka kwa Meneja wa Biashara Zanzibar wa Benki ya NMB, Bi. Naima Said Shaame, wakati wa Mkutano wa Watendaji Wakuu na Wenyeviti wa Bodi wa Taasisi za Kizanzibari uliofanyika Golden Tulip Airport Hotel, Zanzibar. Kushoto ni Mkuu wa Idara ya Biashara za Serikali wa NMB, Bi. Vicky Bishubo. Zawadi hiyo ilitolewa kama ishara ya kuthamini uongozi wa Rais Dkt. Mwinyi katika kukuza uchumi wa Zanzibar na kuimarisha mazingira wezeshi kwa biashara na uwekezaji.








-Minara 2,454, Intaneti Bure na Mapinduzi ya Kidigitali Vijijini

Na Janeth Raphael MichuziTv 

Katika kipindi ambacho dunia inakimbilia kwenye uchumi wa kidigitali, Tanzania imeendelea kuchukua hatua kubwa kuhakikisha wananchi wake hawaachwi nyuma katika mapinduzi ya teknolojia ya mawasiliano. Nyuma ya mafanikio hayo kuna mchango mkubwa wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote nchini (UCSAF), taasisi inayotekeleza dhamira ya kuhakikisha huduma za mawasiliano zinawafikia Watanzania wote bila kujali jiografia ya maeneo wanayoishi.

Kwa miaka ya hivi karibuni, UCSAF imekuwa mhimili muhimu katika kuunganisha jamii za vijijini na maeneo ambayo kwa muda mrefu yalikuwa hayana huduma za uhakika za simu na intaneti. Kupitia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kimkakati, maelfu ya wananchi sasa wanaweza kuwasiliana kwa urahisi, kupata taarifa muhimu, kufanya biashara na hata kupata huduma za kijamii kupitia mifumo ya kidigitali.

Miongoni mwa mafanikio makubwa yaliyopatikana ni ujenzi wa minara 2,454 ya mawasiliano katika maeneo mbalimbali nchini. Minara hiyo imewezesha huduma za simu na intaneti kufika katika vijiji na maeneo ya pembezoni yaliyokuwa hayana kabisa mawasiliano au yaliyokuwa na mtandao hafifu. Hatua hiyo imefungua ukurasa mpya kwa wananchi wa maeneo hayo, ambapo sasa wanaweza kuwasiliana kwa urahisi na kupata huduma muhimu kwa wakati.

Kupitia uwekezaji huo, sekta mbalimbali zimeanza kunufaika moja kwa moja. Wakulima na wafugaji sasa wanapata taarifa za masoko, hali ya hewa na mbinu bora za uzalishaji kupitia simu zao. Wafanyabiashara wadogo wameongeza wigo wa biashara kwa kutumia huduma za kifedha mtandaoni, huku wanafunzi na walimu wakianza kunufaika na upatikanaji wa taarifa na maudhui ya kielimu kupitia intaneti.

Mbali na ujenzi wa minara, UCSAF pia imeendelea kusambaza huduma ya intaneti bure katika maeneo muhimu ya kijamii. Huduma hiyo imefungwa katika shule, vyuo, hospitali pamoja na maeneo mengine ya umma kwa lengo la kuwapa wananchi fursa ya kutumia teknolojia katika kujifunza, kufanya tafiti na kupata taarifa mbalimbali muhimu.

Katika sekta ya elimu, uwepo wa intaneti umeanza kubadilisha namna wanafunzi wanavyojifunza. Vijana wengi waliokuwa wakitegemea vitabu pekee sasa wana uwezo wa kupata maarifa kutoka sehemu mbalimbali duniani kupitia mifumo ya kidigitali. Walimu nao wamepata fursa ya kuboresha ufundishaji kwa kutumia nyenzo za kisasa zinazopatikana mtandaoni.

Sekta ya afya nayo imeendelea kunufaika na maboresho hayo ambapo baadhi ya vituo vya afya na hospitali zimeanza kutumia mifumo ya kidigitali katika utoaji wa huduma. Madaktari wanaweza kufanya mawasiliano ya haraka, kutuma taarifa muhimu za kitabibu na hata kupata ushauri kutoka maeneo mengine kwa urahisi zaidi kuliko ilivyokuwa hapo awali.

Katika kuendana na kasi ya maendeleo ya teknolojia duniani, UCSAF imekuwa sehemu muhimu ya safari ya Tanzania kuelekea uchumi wa kidigitali. Kupitia miradi yake, wananchi wengi zaidi wanaingia kwenye matumizi ya teknolojia, jambo ambalo linaongeza ushiriki wao katika shughuli za kiuchumi, kijamii na hata kiutawala.

Aidha, mafanikio hayo yanaendelea kusaidia kupunguza pengo la kidigitali kati ya mijini na vijijini. Kwa muda mrefu wananchi wa maeneo ya vijijini walikuwa nyuma katika upatikanaji wa huduma za mawasiliano na intaneti, hali iliyokuwa ikikwamisha maendeleo katika nyanja mbalimbali. Leo hii, kupitia uwekezaji wa UCSAF, hali hiyo inaendelea kubadilika kwa kasi kubwa.

Pamoja na mafanikio hayo, bado matarajio ya wananchi ni kuona huduma za mawasiliano zinaendelea kuboreshwa zaidi ili kufikia maeneo mengi zaidi nchini. Kasi ya ukuaji wa teknolojia duniani inaifanya sekta ya mawasiliano kuwa mhimili mkubwa wa maendeleo ya taifa lolote, hivyo uwekezaji unaofanywa sasa unaonekana kuwa msingi muhimu wa Tanzania ya kisasa na yenye ushindani katika ulimwengu wa kidigitali.

Kwa ujumla, UCSAF imeendelea kuonyesha kuwa mawasiliano si anasa tena, bali ni hitaji muhimu la maendeleo ya jamii. Kupitia minara ya mawasiliano, huduma za intaneti bure na miradi mingine ya kidigitali, taasisi hiyo imekuwa daraja linalounganisha Watanzania wengi na fursa za dunia ya kisasa.





📍Ruvuma

Uanzishwaji wa masoko rasmi ya madini pamoja na matumizi ya mfumo wa bei elekezi mkoani Ruvuma, umetajwa kupunguza kwa kiasi kikubwa vitendo vya utoroshaji wa madini huku ukiongeza mapato ya Serikali na kuwanufaisha wachimbaji wadogo.

Mkoa wa Ruvuma kwa sasa una masoko rasmi ya madini mawili likiwemo Soko la Dhahabu na Vito la Songea Mjini pamoja na Soko la Dhahabu na Vito Tunduru, lililozinduliwa rasmi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan Septemba 26, 2024.

Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Ruvuma, Mhandisi Alphonce Bikulamchi, amesema mafanikio hayo yametokana na maboresho yaliyofanywa na Serikali katika usimamizi wa biashara ya madini kupitia masoko rasmi yenye uwazi na ushindani wa kibiashara.

Amesema kabla ya kuanzishwa kwa masoko hayo, baadhi ya wachimbaji walikosa maeneo rasmi ya kuuza madini yao hali iliyochochea biashara holela na utoroshaji wa madini, jambo lililoikosesha Serikali mapato na kuwafanya wachimbaji wadogo kuuza madini yao kwa bei isiyo na tija.

“Kwa sasa wachimbaji wanapata taarifa sahihi za bei elekezi za madini yao, jambo ambalo limeongeza uwazi, kuondoa mianya ya udanganyifu na kuongeza imani katika biashara ya madini,” amesema Mhandisi Bikulamchi.

Ameeleza kuwa uwepo wa wanunuzi kutoka ndani na nje ya nchi katika masoko hayo umeongeza ushindani wa bei na kuwawezesha wachimbaji kuuza madini yao kwa thamani inayostahili.

Aidha, amesema Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya biashara ya madini kwa kuimarisha usimamizi wa masoko na kutoa elimu kwa wachimbaji ili kuhakikisha sekta hiyo inaendelea kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa pamoja na maendeleo ya wananchi.

Kwa mujibu wa Mhandisi Bikulamchi, hatua hiyo pia imeongeza ushiriki wa wachimbaji wadogo katika uchumi rasmi na kusaidia kudhibiti vitendo vya utoroshaji wa madini mkoani Ruvuma.









*Yampokea bondia maarufu duniani Terence Crawford ,kumpeleka katika vivutio vya utalii

Na Said Mwishehe,Michuzi TV


MKURUGENZI wa Bodi ya Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), Ephraim Mafuru amesema mkakati wa bodi hiyo ni kuendelea kuwatumia watu mashuhuri ambao wanavipaji na ushawishi mkubwa kuisemea mema Tanzania lengo likiwa kuunganisha utalii wa michezo ili kuongeza watalii nchini.

Mafuru ameyasema hayo leo Mei 24,2026 katika Uwanja wa Ndege wa Kimataita wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam wakati wa mapokezi wa Bondia maarufu kutoka Marekani Terence Crawford ambaye hajawahi kupoteza pambano lolote na akiwa nchini atatembelea vivutio vya utalii nchini.

“Mmeshuhudia Bodi ya Utali Tanzania imeweza kumkaribisha kwa mara ya kwanza nchini Tanzania bondia maarufu kabisa duniani Terence Crawford,akiwa hapa nchini tumemuandalia ziara ya wiki nzima kutembelea vivutio vya utalii.

“Tunafanya hivyo ili kuwatumia watu mashuhuri ambao wana vipaji na ushawishi mkubwa kwa ajili ya kuisemea mema Tanzania lengo likiwa kuunganisha mazao ya utalii wa michezo ili yaongezee wageni kuja nchini kutalii.

“Mbali na utalii wa wanyamapori, utalii wa fukwe ,utalii wa mikutano, utalii wa utamaduni ,sasa Wizara ya Maliasili na Utalii imejikita kusaidia utalii wa michezo,”amesema.

Amefafanua kama ilivyoshuhudiwa kulikuwa na mchezaji bora kabisa aliyewahi kuchezea timu ya Manchester United na pia alichezea timu ya Taifa ya Uingereza Rio Ferdinand ameondoka nchini juzi leo amekuja bondia Terence Crawford ambaye hajawahi kupigwa shindano lolote ,

Mafuru amesema bodi ya utalii itampeleka bondia huyo Serengeti , Ngorongoro , Zanzibar na Tarangire sambamba na kukutana na viongozi mbalimbali.”Tunataka tumpige shule ya utalii wa Tanzania na akiondoka akaiongelee mema nchi yetu pendwa ya Tanzania.”









Na Mwandishi Wetu, Tanga

CHAMA cha National League for Democracy (NLD), kimeitaka Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa nchini kutosita kuvifuta au kuvifungia vyama vyote vya siasa vinavyokiuka sheria na kuhatarisha amani ya nchi, kikitaka wanasiasa wanaoshindwa kufuata sheria wajitoe na kuwa wanaharakati.

Wito huo umetolewa Leo mei 25 jijini Tanga na Katibu Mkuu wa NLD, Doyo Hassan Doyo, wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu hali ya kisiasa nchini, kufuatia hatua ya CHADEMA kuitisha maandamano ya nchi nzima kushinikiza kuachiwa kwa Mwenyekiti wao, Tundu Lissu.

Doyo alisema Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa inafanya kazi kwa mujibu wa Sheria ya Vyama vya Siasa ya mwaka 2019, na kuwataka Watanzania kuacha tabia ya kulalamika na kuishutumu mamlaka hiyo kuwa inaegemea upande mmoja pale inapochukua hatua za kisheria.

"Msajili haipendelei chama chochote, kila chama kinaonywa na kuadhibiwa kadiri kinavyofanya makosa. Baada ya CHADEMA kutoa kauli zinazoashiria uvunjifu wa amani, waliandikiwa barua ya kujieleza, lakini hata CCM nao waliandikiwa barua kufuatia kauli ya Mwenyekiti wa UWT, Mary Chatanda, aliyesema angekuwa Rais kwa dakika moja angekifuta CHADEMA. Hii inathibitisha msajili haangalii uso wa mtu," alisema Doyo.

Katibu Mkuu huyo alisisitiza kuwa vyama vyote vimesajiliwa kisheria, hivyo vinapaswa kuendesha shughuli zake ndani ya kanuni zilizowekwa na sio kujiendesha kama makundi ya harakati mitaani.

Aliongeza kuwa, pamoja na kelele na maneno mengi ya kisiasa, CHADEMA wametekeleza takwa la kisheria kwa kujibu barua ya msajili, na sasa ni jukumu la Ofisi ya Msajili kuweka wazi kwa umma kile ambacho chama hicho kimekijibu ili kuondoa sintofahamu.

"Kama kuna chama kinataka kujiendesha tofauti na sheria, wajitoe rasmi tujue ni wanaharakati. Kulinda amani ya nchi hii sio jukumu la Chama Tawala (CCM) pekee, ni jukumu letu sote wanasiasa kufanya siasa za kisheria, alieleza.

Doyo alirejea kumpongeza kwa dhati Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa anayofanya ya kuleta umoja na utulivu kupitia falsafa yake ya maridhiano, ambayo imetoa uwanja mpana kwa vyama vyote kufanya siasa za kistaarabu.

Akizungumzia ziara yake mkoani Tanga, Doyo alisema mara ya mwisho kufika mkoani hapa ilikuwa ni wakati wa kuzindua kampeni za Urais mwaka 2025, na sasa amerejea maeneo hayo kwa ajili ya kuimarisha na kukisuka chama chake kuelekea uchaguzi mkuu wa ndani wa NLD unaotarajiwa kufanyika mwakani (2027).




WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuwekeza katika miradi ya barabara nchini kwa kuwa ndiyo msingi wa kufungua uchumi, kurahisisha usafirishaji wa mazao na kuchochea maendeleo ya wananchi vijijini na mijini.

“Hizi kilomita 17 zilizobaki kuelekea Dabaga ni eneo muhimu sana la uzalishaji, hivyo Serikali itaendelea kuweka mkazo kuhakikisha eneo hilo linafunguliwa kwa kiwango cha lami,” amesema Dkt. Mwigulu.

Dkt. Mwigulu amesema hayo leo Jumapili, Mei 24, 2026 alipokagua mradi wa ujenzi wa Barabara ya Iringa (Ipogolo) – Kilolo yenye urefu wa kilomita 33.61 kwa kiwango cha lami chini ya Programu ya RISE (Barabara kwa Maendeleo na Fursa za Kiuchumi na Kijamii) katika Wilaya ya Kilolo mkoani Iringa.

Amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kutekeleza miradi ya kimkakati ya miundombinu kwa lengo la kuimarisha shughuli za kiuchumi na kuboresha huduma za usafiri kwa wananchi.

Aidha, Waziri Mkuu amesema Serikali imekubaliana kuhakikisha miradi yote iliyoanza inakamilishwa kwanza sambamba na kuendelea kutoa fedha za utekelezaji kwa miradi iliyosainiwa mikataba lakini haikupata malipo ya awali.

“Tunahakikisha kwanza tunakamilisha miradi ambayo ilikuwa imeanza, iliyosainiwa lakini haikupata malipo ya awali na ile ambayo wakandarasi walishapatikana ili wananchi waanze kunufaika na miradi hiyo,” amesema.

Kadhalika, amesema Serikali imeongeza kasi ya utekelezaji wa miradi mingine baada ya kukamilisha baadhi ya miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo Bwawa la Julius Nyerere, reli ya kisasa ya SGR pamoja na Daraja la Kigongo – Busisi.

“Tuliamua kwanza tumalize miradi mikubwa iliyokuwa imefikia hatua nzuri ili ianze kusaidia uchumi wa nchi. Sasa tunaongeza nguvu kwenye miradi mingine iliyokuwa imepunguza kasi ya utekelezaji wake,” amesema.

Amesema mradi huo wa barabara una umuhimu mkubwa kwa wananchi wa Kilolo kutokana na eneo hilo kuwa miongoni mwa maeneo yenye uzalishaji mkubwa wa mazao ya kilimo mkoani Iringa.

Kwa upande wake, Mbunge wa Kilolo, Rita Kabati amesema wananchi wa Kilolo wameendelea kunufaika na uwekezaji mkubwa wa Serikali katika sekta ya miundombinu huku akiishukuru Serikali kwa kuendelea kutatua changamoto za usafiri katika wilaya hiyo.

“Uchumi wa Kilolo unategemea barabara. Maeneo mengi hayapitiki wakati wa mvua na suluhisho lake ni barabara za lami,” amesema Rita Kabati.

Naye Kaimu Meneja wa TANROADS Mkoa wa Iringa, Mhandisi Hosea Machaka amesema mradi huo wenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 60.14 umefikia asilimia 96 ya utekelezaji na tayari umekabidhiwa kwa matumizi.

Amesema mradi huo umehusisha ujenzi wa daraja la Ndiwili lenye urefu wa mita 40, makalavati makubwa 13, makalavati madogo 54 pamoja na njia za watembea kwa miguu na waendesha baiskeli kwa lengo la kuimarisha usalama wa watumiaji wa barabara.

Aidha, amesema wananchi 596 waliopitiwa na mradi huo walilipwa fidia ya zaidi ya shilingi bilioni 2.54 huku ajira 393 zikizalishwa ambapo asilimia 95 ya ajira hizo zilitolewa kwa wananchi wa eneo husika.








Na Janeth Raphael MichuziTv - Iringa


WAZIRI Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka wananchi nchini kuacha kufanya mambo kwa mazoea na kuaminiana pekee, hasa katika masuala ya ardhi na mali, akisema kupungua kwa uaminifu katika jamii kunachochea migogoro mikubwa ndani ya familia na jamii kwa ujumla.

Dkt. Mwigulu ametoa kauli hiyo leo wilayani Kilolo mkoani Iringa wakati akihutubia wananchi katika mwendelezo wa ziara yake ya kikazi mkoani humo, ambapo amesisitiza umuhimu wa wananchi kufuata taratibu rasmi za kisheria katika umiliki, uazimishaji na makubaliano mbalimbali ya mali.

Amesema kuwa wananchi wengi wamekuwa wakifanya makubaliano ya ardhi kwa mazoea bila kuyaweka kisheria, hali ambayo imekuwa chanzo kikubwa cha migogoro pindi mmoja wa wahusika anapofariki dunia au kutokea sintofahamu ndani ya familia.

“Mtu anaazimisha shamba kutoka kwa familia fulani, lakini wakabaki wanaaminiana tu bila kuandika makubaliano yoyote. Sasa mwenye shamba anapofariki au aliyekodishwa akitaka kubaki na eneo hilo, migogoro inaanza. Mkifika mahakamani inakuwa vigumu kushinda kwa sababu hakuna nyaraka wala utaratibu wa kisheria uliofuatwa,” amesema Dkt. Mwigulu.

Ameeleza kuwa mabadiliko ya maisha na kupungua kwa uaminifu katika baadhi ya maeneo ya jamii yanapaswa kuwa somo kwa wananchi kuona umuhimu wa kuweka kumbukumbu rasmi za kila makubaliano yanayohusu ardhi au mali nyingine muhimu.

Aidha, Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kusimamia na kufuatilia migogoro ya ardhi nchini kwa karibu ili kuhakikisha wananchi wanapata haki zao pamoja na suluhisho la kudumu la migogoro hiyo.

Amesisitiza kuwa kufuata sheria na taratibu kutasaidia kupunguza kesi nyingi mahakamani, kuimarisha amani ndani ya familia na kulinda haki za pande zote zinazohusika katika umiliki wa mali.

Dkt. Mwigulu pia amewahimiza viongozi wa serikali za mitaa pamoja na wataalamu wa ardhi kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kuandikisha mikataba na kumiliki ardhi kwa mujibu wa sheria ili kuepusha migogoro inayoweza kuzuilika.

Kwa upande wao, baadhi ya wananchi waliohudhuria mkutano huo wamepongeza kauli ya Waziri Mkuu wakisema changamoto za migogoro ya ardhi zimekuwa zikisababisha migawanyiko ndani ya familia na hata kuchelewesha maendeleo katika jamii.

Ziara ya Dkt. Mwigulu mkoani Iringa inaendelea ambapo pamoja na mambo mengine anatarajiwa kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo na kuzungumza na wananchi kuhusu utekelezaji wa shughuli za Serikali katika maeneo tofauti ya mkoa huo.




Top News