Na Janeth Raphael MichuziTv

Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) kwa kushirikiana na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) zimeandika historia baada ya kufanikisha kwa mara ya kwanza upasuaji wa kuziba matundu ya moyo kwa watoto kutoka nchini Burundi, hatua inayotajwa kuwa mafanikio makubwa katika kuimarisha huduma za kibingwa na kukuza tiba utalii nchini Tanzania.

Mafanikio hayo yametangazwa na Mkurugenzi wa Hospitali ya Benjamin Mkapa, Prof. Abel Makubi, wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma ambapo amesema ushirikiano kati ya BMH na JKCI unaendelea kuzaa matokeo chanya na utaimarishwa zaidi ili kuongeza wigo wa huduma za kibingwa na ubingwa bobezi kwa Watanzania pamoja na wagonjwa kutoka mataifa jirani.

Prof. Makubi amesema hatua hiyo ni ya kihistoria kwa kuwa ndiyo mara ya kwanza kwa taasisi hizo mbili kushirikiana kuwafanyia watoto kutoka nje ya Tanzania upasuaji wa moyo, jambo linaloonesha uwezo wa nchi katika kutoa huduma za matibabu zinazokidhi viwango vya kimataifa.

Amesema Tanzania imejipanga kuhakikisha wagonjwa kutoka ndani na nje ya mipaka yake wanapata huduma bora za kibingwa bila kulazimika kusafiri kwenda mataifa ya mbali kutafuta matibabu yanayopatikana hapa nchini.

"Kwa miaka mingi tumekuwa tukishuhudia wagonjwa wakisafiri kwenda nje kwa huduma ambazo sasa zinaweza kutolewa nchini kwa ufanisi na kwa gharama nafuu zaidi. Dhamira yetu ni kuona Tanzania inakuwa kitovu cha huduma za matibabu kwa ukanda wa Afrika Mashariki na kwingineko," amesema Prof. Makubi.

Akizungumzia hali za wagonjwa hao, Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Moyo na Kifua, Dk. Ahmed Toure, amesema watoto waliopatiwa matibabu walizaliwa na matatizo ya kimaumbile ya moyo yaliyokuwa yakihitaji upasuaji maalumu ili kurekebisha mfumo wa mzunguko wa damu.

Amefafanua kuwa baadhi ya watoto wenye matatizo hayo huzaliwa na hitilafu kwenye mishipa ya moyo inayosababisha damu kutosambaa ipasavyo kwenda kwenye mapafu na sehemu nyingine za mwili, hali ambayo inaweza kusababisha madhara makubwa endapo matibabu hayatatolewa mapema.

Kwa mujibu wa Dk. Toure, watoto wengi huanza kuonesha athari kubwa wanapofikisha umri wa miezi sita hadi mwaka mmoja, hivyo uchunguzi wa mapema na upasuaji kwa wakati ni muhimu katika kuongeza nafasi ya kuishi maisha marefu na yenye afya.

Naye Mratibu wa Tiba Utalii Tanzania, Dk. Asha Mahita, amesema mafanikio hayo yanaendana na malengo ya Serikali kupitia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambayo inalenga kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha huduma za tiba utalii katika ukanda wa Afrika.

Amesema kuwapokea na kuwatibu wagonjwa kutoka Burundi ni ushahidi kuwa uwezo wa wataalamu wa afya nchini unaendelea kuimarika na kwamba huduma zinazotolewa sasa zinavutia wagonjwa kutoka mataifa mengine.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuhakikisha wagonjwa wanaendelea kufuatiliwa baada ya upasuaji ili kuhakikisha wanapata nafuu kamili na kuendelea kuishi maisha yenye afya.

Kwa upande wake, Daktari Bingwa Mbobezi wa Upasuaji wa Moyo kwa Watoto kutoka JKCI, Dk. Godwin Godfrey, amesema ushirikiano kati ya taasisi hizo mbili umeongeza uwezo wa wataalamu kubadilishana uzoefu na kuendelea kuboresha huduma za kibingwa nchini.

Ameeleza kuwa ushirikiano huo unachangia kuwafikia wagonjwa wengi zaidi, kuongeza ujuzi kwa wataalamu wa afya na kuwezesha hata wananchi wasio na uwezo mkubwa wa kifedha kupata huduma za matibabu zenye ubora wa hali ya juu.

Kutoka Burundi, Dkt. Nzitunga Aimee Jean Carmen Octavie wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Gitega ameishukuru Serikali ya Tanzania pamoja na uongozi wa BMH kwa kuwakaribisha na kuwapatia watoto wao matibabu salama.

Amesema mafanikio hayo yanaimarisha zaidi uhusiano wa kihistoria uliopo kati ya Tanzania na Burundi, huku yakitoa matumaini mapya kwa wagonjwa wanaohitaji huduma za kibingwa katika ukanda huo.

Naye mzazi wa mmoja wa watoto waliopatiwa upasuaji, Shedrack Nzigiyimana, amesema ameridhishwa na huduma alizopata mtoto wake na kushukuru wataalamu wa afya pamoja na Serikali ya Tanzania kwa kuwapa fursa ya kupata matibabu yaliyobadili maisha ya mtoto wake.

Amesema ukarimu na ushirikiano kati ya Tanzania na Burundi umewezesha watoto wao kupata huduma muhimu ambazo zingekuwa vigumu kuzipata kwa wakati, huku akieleza matumaini kuwa ushirikiano huo utaendelea kuwasaidia wagonjwa wengi zaidi kutoka nchi zote mbili.











Na Pamela Mollel,Arusha.

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji (Mb), amemtaka Kamishna mpya wa Uhifadhi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Massana Gibril Mwishawa, kuimarisha utendaji wa shirika hilo kwa kuhakikisha sekta ya uhifadhi na utalii inaendelea kutoa mchango mkubwa katika maendeleo ya taifa

Akizungumza jijini Arusha wakati wa hafla ya kumuapisha Kamishna huyo, Waziri Kijaji amesema uongozi mpya unapaswa kuelekeza nguvu katika kuboresha miundombinu ya hifadhi, kuongeza fursa za uwekezaji, kuanzisha bidhaa mpya za utalii na kusimamia mapato kwa ufanisi ili kuongeza mchango wa sekta hiyo kwenye uchumi wa nchi

Pia alisisitiza umuhimu wa kujenga mahusiano mazuri na wananchi wanaozunguka maeneo ya hifadhi, akieleza kuwa ushirikiano wao ni nguzo muhimu katika kulinda rasilimali za taifa

Aidha, alimwelekeza Kamishna kuhakikisha nidhamu, uadilifu, weledi na ustawi wa watumishi wa TANAPA vinaendelea kupewa kipaumbele

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya TANAPA, Mkuu wa Majeshi Mstaafu Jenerali George Waitara, amesema bodi itaendelea kushirikiana na menejimenti ya shirika hilo kwa kutoa ushauri na miongozo itakayosaidia kufanikisha malengo ya uhifadhi na maendeleo ya utalii nchini.

Aliongeza kuwa uwazi katika uendeshaji wa shughuli za shirika pamoja na utoaji wa mrejesho kwa watumishi wa ngazi mbalimbali ni muhimu katika kuongeza ufanisi na kufikia malengo yaliyowekwa

Naye Kamishna wa Uhifadhi, Massana Gibril Mwishawa, amesema ataiongoza TANAPA kwa kuzingatia misingi ya uwajibikaji, uzalendo, uadilifu na weledi, huku akisisitiza kuwa hifadhi za taifa zina nafasi muhimu katika kulinda bioanuwai, kuchochea uchumi na kusaidia utekelezaji wa miradi ya maendeleo kupitia mapato yatokanayo na utalii.

Aliongeza kuwa anamshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kumteua kushika nafasi hiyo, akiahidi kushirikiana kwa karibu na watumishi wote wa TANAPA ili kuendelea kuimarisha mafanikio ya taasisi hiyo.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi wa taasisi mbalimbali za uhifadhi, akiwemo NCAA, TFS na TAWA, pamoja na viongozi wa Serikali, wadau wa sekta ya uhifadhi na utalii, viongozi wa dini, maafisa na askari wa TANAPA.







Na Seif Mangwangi, Michuzi TV Arusha

SERIKALI imesema Mwitikio wa vijana kutaka kukopeshwa fedha kwaaji li ya kuanzisha biashara umekuwa mkubwa na wa kutia moyo baada ya baadhi ya masharti magumu yaliyokuwa yakiwashinda vijana kuondolewa.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa programu ya Kitaifa ya utoaji wa mikopo kupitia programu ya billioi 200 chini ya mfuko wa maendeleo ya vijana leo 9 Julai 2026,Jijini Arusha, Waziri wa nchi ofisi ya Rais Vijana, Joel Nananuka amesema miongoni mwa changamoto zilizokuwa zikilalamikiwa ni riba kubwa kwa wakopaji.

“Riba ilikuwa ni changamoto, na Sasa riba imeondolewa mtu akishapata mikopo na kulipa bima basi atapata mikopo wake, pia kulikuwa na changamoto ya mikopo kurejesha mapema, tunataka mtu akipata fedha aanze kufanyia kazi ndipo aanze kurejesha, mwongozo mpya ni kwamba watakaa na mkopo kwa miezi mitatu kabla ya kuanza kurejesha,” amesema.

Amesema changamoto nyingine iliyofanyiwa mabadiliko ni mtu mmoja mmoja kupata fedha kama alivyoomba badala ya kuwa katika kikundi ndio update fedha hizo kama ilivyokuwa hapo awali.

“ Ilikuwa fedha zinatolewa kwa vikundu pekee na sio mtu mmoja mmoja lakini sasa hivi kama tulivyoagizwa na Mheshimiwa Rais Samia tuondoe vikwazo vyote, basi awamu hii vijana wengi watapata mkopo Kwa namna alivyoomba bila kupitia kikundi,” amesema.

Amesema baada ya kutatuliwa Kwa changamoto hizo, jumla ya maombi 30,384 yalipokelewa kutoka maeneo mbalimbali nchini yakihusisha sekta za kilimo, mifugo, uvuvi, viwanda vidogo, biashara, ubunifu, teknolojia na huduma mbalimbali.

“ Takwimu hizi zinaonesha wazi kuwa vijana wa Tanzania si wavivu kama ambavyo wakati mwingine imekuwa ikidaiwa;

badala yake, wanahitaji mazingira yanayowapa fursa ya kuonesha uwezo wao,” amesema Nanauka na kuongeza:

“Baada ya mchakato wa kina wa tathmini uliozingatia vigezo vilivyowekwa, kwa awamu ya kwanza tunaenda kuwezesha miradi ya vijana yenye thamani ya Shilingi Bilioni 8 kupitia Mfuko wa Maendeleo ya vijana unapojaribiwa na Ofisi ya Rais - Maendeleo ya vijana,” amesema.

Amesema katika uzinduzi wa programu hiyo, katika Mkoa wa Arusha mikopo ya shilingi milioni 730 itatolewa ambapo milioni 500 zitaenda katika utafiti na utengenezaji wa dawa za binadamu, Milioni 130 zitaenda katika kiwanda cha vijana kinachotengeneza chaki zisizotoa vumbi na milioni 100 zitaenda kwa viundi vya Mama na Baba Lishe.

“ Hii ni hatua ya mwanzo ambayo itaendelea kupanuliwa kadri fedha zitakavyopatikana na tathmini za utekelezaji zitakavyoendelea kuonesha mafanikio,” amesema.

Amesema fedha hizo ni za uwekezaji wa Taifa kwa vijana wake na kwamba Serikali imewaamini na imeamua kuwekeza kwa vijana kwa matarajio kwamba watazitumia kuongeza uzalishaji, kupanua biashara, kuanzisha viwanda vidogo, kuongeza thamani ya bidhaa na kuzalisha ajira kwa vijana wengine.

“Napenda kuwasisitiza kuwa mafanikio ya programu hii hayatapimwa kwa kiwango cha fedha kilichotolewa, bali kwa matokeo yatakayopatikana. Tunataka kuona biashara zenye tija, ongezeko la mapato ya kaya, ajira mpya, ukuaji wa kampuni za vijana na mchango mkubwa wa sekta ya vijana katika pato la Taifa, “ amesema na kuongeza:

“Hivyo basi, nawasihi mtumie fedha hizi kwa malengo yaliyokusudiwa; wekeni mifumo mizuri ya usimamizi wa fedha; tunzeni kumbukumbu za biashara zenu; zingatieni misingi ya utawala bora wa biashara; na hakikisheni mnarejesha mikopo kwa wakati. Nidhamu ya fedha ndiyo msingi wa mafanikio ya biashara yoyote duniani.” Amesema.

Awali Mkuu wa Mkoa wa Arusha CPA Amos Makala amesema vijana wa Arusha wanajitambua na hawachezi na fursa na kwamba Kwa juhudi wanazoendelea nazo ana uhakika kesho yao itakuwa njema.

Mwakilishi wa benki ya CRDB, Meneja wa Benki hiyo tawi la Meru Arusha, Haika Mawalla amesema CRDB Bank inajivunia kuaminiwa na Serikali kupewa jukumu la kusimamia utekelezaji wa mpango huo wa uwezeshaji wa vijana nchini kote.

“ Hili ni jukumu kubwa na tunalipokea kwa uzito, uadilifu na uwajibikaji. Tumejipanga kuhakikisha huduma hii inawafikia vijana wengi iwezekanavyo kwa uwazi, ufanisi na weledi,” amesema.

Amesema mbali na kutoa mikopo, CRDB itaendelea kuwajengea vijana uwezo kupitia elimu ya fedha, usimamizi wa biashara na matumizi sahihi ya mikopo na kwamba wanaamini kuwa mchanganyiko wa mtaji, maarifa na nidhamu ya fedha ndio msingi wa mafanikio ya biashara na ujasiriamali endelevu.

“Tunawasihi vijana wote kuitumia fursa hii kwa ubunifu, uwajibikaji na uaminifu. Mikopo hii ni chachu ya maendeleo; itumike kuanzisha na kukuza miradi yenye tija, kuongeza ajira na kuinua uchumi wa familia na Taifa kwa ujumla,” amesema.






Na Janeth Raphael MichuziTv

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema Watanzania wanahitaji amani, usalama na utulivu badala ya vurugu na mivutano ya kisiasa, akisisitiza kuwa mazingira hayo ndiyo msingi wa Serikali kuendelea kutoa huduma bora za kijamii, kukuza uchumi na kuongeza fursa za ajira kwa wananchi.

Rais Samia ametoa kauli hiyo leo Alhamisi, Julai 9, 2026, visiwani Zanzibar wakati wa hafla ya kushuhudia utiaji saini wa Tamko la Pamoja la Maridhiano ya Kisiasa kati ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na ACT Wazalendo.

Amesema maridhiano ya kisiasa hayapaswi kutafsiriwa kama ishara ya udhaifu, bali ni alama ya ukomavu wa kisiasa unaojenga msingi wa umoja, kuheshimiana na ushirikiano miongoni mwa viongozi wenye mitazamo tofauti kwa maslahi ya taifa na wananchi.

Kwa mujibu wa Rais Samia, hatua hiyo inafungua ukurasa mpya wa kuimarisha mshikamano, amani na utulivu nchini, hususan Zanzibar, huku akihimiza siasa kujengwa katika misingi ya hoja, heshima na ustaarabu badala ya chuki, migawanyiko na mivutano isiyo na tija.

Amesema migogoro na siasa za chuki huzuia maendeleo, lakini maridhiano na siasa za staha huweka mazingira bora ya utekelezaji wa mipango ya maendeleo na kuboresha ustawi wa wananchi.

Rais Samia pia amezitaka pande zote zinazohusika na maridhiano hayo kuheshimu makubaliano yaliyofikiwa, kuendelea na mazungumzo kwa uwazi na kujenga imani ili kulinda umoja, amani na usalama wa taifa.

Akihitimisha hotuba yake, Rais Samia amesisitiza umuhimu wa kudumisha mshikamano uliojengwa kupitia maridhiano hayo.

"Hekima tuliyoionesha leo ikalindwe kwa matendo mema ya kesho, na imani tuliyoijenga kwa muda mrefu isiangushwe kwa maneno au mienendo isiyo na tija," amesema Rais Samia.

















JESHI la Polisi Mkoa wa Kilimanjaro linamshikilia mtu mmoja aitwaye Beatrice Urassa (59) kwa tuhuma za mauaji ya watu wanne ambao walifariki dunia kwa nyakati tofauti wakiwa wanapatiwa matibabu katika hospitali ya Machame Wilayani Hai.

Akithibitisha kukamatwa kwake, Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro, SACP Saimon Maigwa aliwataja waliofariki dunia ni Hamida Hamis Kweka (26), Robson Edson Meena (34), Ismail Exaud Uronu (34) na Kamama Exaud Uronu (45) wote wakazi wa kitongoji cha kinyaro, kata ya Mnadani, wilaya ya Hai na Mkoa wa Kilimanjaro.

Kamanda Maigwa alisema kuwa, uchunguzi wa awali umebaini kuwa, mtuhumiwa huyo anadaiwa kuwapatia dawa za kienyeji watu hao ambao ni ndugu wa familia moja, na kupelekea kufariki dunia wakiwa wanapatiwa matibabu Julai 05 mwaka huu majira ya usiku.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Kilimanjaro linaendelea na uchunguzi kuhusina na tukio hili, pindi utakapokamilika taratibu nyingine za kisheria zitafuata.


ZAIDI ya Bilioni saba (7) zimekamilisha ujenzi wa soko la kimataifa la mazao katika kijiji cha Kanondo halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga mkoani Rukwa.

Akizungumza wakati akikagua eneo la soko la kimataifa la mazao Waziri wa katiba na sheria Juma Homera ameitaka halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga kuanza kutumia soko hilo ifikapo August mosi mwaka huu.

Amewapongeza halmashauri kwa kusimamia na kukamilisha mradi huo huku akiwasisitiza kuendelea kusimamia miradi ya maendeleo kwa uwazi na uadilifu.

Aidha mstahiki meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga Frenk Lupimo ameeleza umuhimu wa soko hilo kuwa linauwezo wa kuchukua tani 19,000 na litasaidia kukuza mapato ya ndani na kukuza uchumi kwa wafanyabiashara watakao tumia soko hilo.

Kwa upande wao wananchi wa eneo hilo wamemshukuru Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa ujenzi wa soko la mazao na kuwa soko hilo linakwenda kutatua changamoto na kuondoa walanguzi waliokuwa wakiwaibia wakulima.

Pia wameeleza kuwa awali walikuwa wakiibiwa na walanguzi kutoka nchi jirani wakitumia vipimo vinavyo waumiza wakulima ambapo kwa kujengwa kwa soko hilo tatizo hilo linakwenda kumalizika kwasababu wakulima na wafanyabiasha watauza na kununua mazao katika soko hilo.




Jane Mwakyoma - Rukwa.

WAKAZI wa kata ya Msua Manispaa ya Sumbawanga mkoani Rukwa wameishukuru serikali ya awamu ya sita kwa ujenzi wa shule ya msingi Kisiwani inayowasaidia wanafunzi wa eneo hilo kupata elimu karibu na makazi yao.  

Wakizungumza baada ya waziri wa katiba na sheria Juma Homera kutembelea na kukagua ujenzi unaoendelea shuleni hapo wananchi wamesema ujenzi wa shule hiyo unasaidia watoto kupata elimu karibu na makazi yao ukilinganisha na hapo awali walikuwa wakifuata elimu hiyo zaidi ya km 3 hali iliyokuwa ikihatarisha usalama wa watoto hao.

Akimwakilisha mwalim mkuu wa shule ya msingi Kisiwani Efrahim Kimario amesema walipokea fedha za ujenzi zaidi ya Milioni 329 ikiwa majengo sita yamekamilika na tayari yanatumika huku jengo la utawala likiwa katika hatua ya umaliziaji kuhakikisha watoto wa eneo hilo wanaendelea kupata elimu ya msingi shuleni hapo.

Aidha amesema ujenzi wa shule hiyo unatumia mfumo wa Force Account ambapo alimshukuru Mbunge wa jimbo la Sumbawanga mjini Aishi Khalfan Hilali na Dtk. Samia Suluhu Hassan kwa jitihada walizofanya kuhakikisha shule inajengwa na watoto wanapata elimu ya uhakika.

Kwa upande wake Waziri wa katiba na sheria Juma Homera amepongeza halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga kwa usimamizi wa mradi na kuhakikisha baadhi ya majengo yanakamilika na kuendelea kutoa huduma kwa wanafunzi.

Pia Homera amewataka viongozi wa serikali nchini kusimamia kikamilifu miradi ya maendeleo na kuhakikisha inakamilika kwa wakati ili kuepusha migogoro ya wananchi na serikali.



Tukio la Ngorongoro kuonesha vivutio vya utalii mubashara kupitia runings kubwa iliyofungwa katika banda la Wizara ya Maliasili na Utalii

limevutia wananchi wengi wanaotembelea  maonesho ya 50 ya biashara ya kimataifa jijini  Dar es Salaam kwa kuoneshwa maajabu yaliyopo Ngorongoro hususan Kreta ya Ngorongoro, makundi ya wanyama mbalimbali ikijumuisha pundamilia, nyumbu, swala, nyati na wanyama adimu kama  faru, simba, tembo na  na  chui na kujihisi kama wapo nyumbani Ngorongoro.

Afisa Uhusiano Mkuu wa Ngorongoro Bw. Walter Mairo ameeleza kuwa  kupitia runinga iliyofungwa viwanja vya maonesho wageni wanaotembelea wanaona wanyama aina mbalimbali ndani ya Kreta, tambarare za Ndutu ambapo maisha ya Nyumbu kuzaliwa, kukua, kusafiri na kurejea na kuanza kizazi kipya kila mwaka

Mairo ameongeza kuwa, matukio mubashara yanaonesha wananchi jinsi teknolojia ya kidigitali na utalii wa asili vinavyoweza kushirikiana kuelimisha, kuburudisha na kuonyesha ushahidi kuwa Ngorongoro si tu hifadhi, bali ni jukwaa la kidunia linalounganisha urithi, biashara na teknolojia sehemu moja.

Karibu Sabasaba timu yetu yenye wabobezi na watopezi imejipanga kukupa  hadhithi za Ngorongoro zitakazokuduwaza kuwa Ngorongoro sio mahali pa kuangalia tu, bali mahali pa kuelewa, kujifunza na kuishi uzoefu usiosahaulika.


Na Janeth Raphael MichuziTv 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, amesema maridhiano ya kisiasa hayapaswi kutafsiriwa kama udhaifu, bali ni ishara ya ukomavu wa kisiasa unaoweka msingi imara wa umoja, amani na kuheshimiana katika jamii.

Akihutubia katika hafla ya utiaji saini wa Tamko la Pamoja la Maridhiano ya Kisiasa Zanzibar iliyofanyika visiwani Zanzibar leo, Alhamisi Julai 9, 2026, Rais Samia alisema viongozi wanaweza kuwa na mitazamo tofauti, lakini wakaunganishwa na dhamira ya kulinda maslahi ya taifa na ustawi wa wananchi.

Ameeleza kuwa maridhiano yanaonyesha uwezo wa viongozi kujadili hoja zinazowatofautisha kwa hekima, huku wakikubaliana katika masuala ya msingi yanayohusu uongozi na maendeleo ya nchi.

Rais Samia alisema hatua hiyo inafungua ukurasa mpya wa kuimarisha umoja, mshikamano, utulivu na amani kwa wananchi wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla, akisisitiza kuwa jitihada hizo zinapaswa kuendelezwa na kuenziwa.

“Hakika jitihada hizi zinahitaji kuendelezwa na kuenziwa. Nimesema jambo hili la kiungwana kwa kuwa uungwana unatufunza siasa za kushindana kwa hekima na si kwa kupaza sauti bila mantiki,” amesema Rais Samia.

Aidha, ametoa wito kwa viongozi na wadau wa siasa kuendelea kujenga utamaduni wa mazungumzo, kuheshimiana na kuweka mbele maslahi ya taifa ili kudumisha amani na kuharakisha maendeleo ya wananchi.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi pamoja na wageni mbalimbali waliohudhuria hafla ya uwasilishaji wa Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, katika viwanja vya Ikulu Zanzibar tarehe 09 Julai, 2026.







Na Mwandishi Wetu
USHIRIKIANO kati ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Japani kupitia Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Japani (JICA) umefungua fursa mpya za maendeleo katika sekta ya kilimo baada ya kutolewa kwa mkopo wa masharti nafuu wenye thamani ya zaidi ya Shilingi trilioni 3.5 kupitia Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB).

Fedha hizo zinatolewa kupitia Wizara ya Fedha chini ya mradi wa Two Step Loan, unaolenga kuongeza upatikanaji wa mitaji kwa sekta ya kilimo kwa kuwawezesha wakulima binafsi, vikundi vya wakulima pamoja na wakulima wadogo na wa kati kupata mikopo yenye masharti nafuu kwa ajili ya kuongeza uwekezaji na uzalishaji.

Akizungumza katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), Afisa Biashara wa TADB anayesimamia miradi ya benki hiyo, Elias Misana, alisema mradi huo unalenga kuchochea ukuaji wa sekta ya kilimo kupitia ufadhili wa mazao matano ya kimkakati ambayo ni mahindi, mpunga, ngano, alizeti na mazao ya bustani.

Alieleza kuwa kupitia mpango huo, mkulima mmoja mmoja ataweza kupata mkopo wa hadi Shilingi milioni 200, huku vikundi vya wakulima na kampuni zinazojihusisha na shughuli za kilimo zikiweza kukopa hadi Shilingi bilioni tatu kwa masharti nafuu.

Misana alisema mpango huo pia umeweka kipaumbele kwa wanawake na vijana wanaojishughulisha na kilimo cha bustani, ambao watanufaika na viwango vya chini vya riba pamoja na muda mrefu na rafiki wa marejesho ya mikopo.

Kwa upande wake, Mratibu Mkuu wa JICA, Veronica Barua, alisema mradi wa Two Step Loan ni matokeo ya ushirikiano wa muda mrefu kati ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Japani unaolenga kuwawezesha wakulima wadogo na wa kati kupata mitaji ya uwekezaji, hususan wale waliokuwa wakikabiliwa na changamoto ya kupata mikopo kutoka taasisi za kifedha.

Alisema upatikanaji wa mitaji hiyo unatarajiwa kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao, kuboresha kipato cha wakulima na kuimarisha mchango wa sekta ya kilimo katika ukuaji wa uchumi wa taifa.

Mradi wa Two Step Loan ulianza kutekelezwa rasmi mwezi Juni mwaka 2025 na unatarajiwa kuendelea hadi mwaka 2029. Kupitia matawi ya TADB na benki washirika nchini kote, maelfu ya wakulima wanatarajiwa kunufaika na mpango huo, hatua itakayochochea usalama wa chakula, kuongeza uzalishaji na kuimarisha maendeleo ya sekta ya kilimo nchini.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam,Albert Chalamila akipata maelezo kutoka kwa Afisa Mtendaji Mkuu wa Yas, Pierre Canton Bacara kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa na kampuni hiyo kwenye Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (SABASABA) mara baada ya kutembelea banda hilo, Banda la Yas limekusanya suluhisho mbalimbali zinazolenga kuboresha maisha ya Watanzania, ikiwemo huduma ya uchunguzi wa macho bure, mpango wa kumiliki simu janja na rauta za 5G kwa mkopo, huduma za intaneti majumbani na kwa wajasiriamali kupitia Yas Fiber, suluhisho kwa wafanyabiashara na taasisi kupitia Yas Business, pamoja na huduma na suluhisho mbalimbali za kifedha kupitia Mixx.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila akizungumza katika  kwenye Banda la Yas katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (SABASABA) wakati alipotembelea Banda hilo.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila akizungumza Mtoto aliyefika na mzazi wake kupata huduma ya Macho katika Banda la Yas  kwenye Banda la Yas katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (SABASABA) wakati Mkuu wa Mkoa huyo  alipotembelea Banda hilo.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila akizungumza na mwananchi   kwenye Banda la Yas katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (SABASABA) wakati alipotembelea Banda hilo.


Top News