Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, akiwa kwenye picha na Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde, pamoja na Mwenyekiti wa Bodi ya Kampuni ya Perseus Mining Limited Bw. Rick Menell mara baada ya mazungumzo yao, Ikulu ya Chamwino, Dodoma tarehe 06 Mei, 2026.

Perseus Mining Limited ni mwekezaji wa Mgodi wa Dhahabu wa Nyanzaga, Wilayani Sengerema, Mkoani Mwanza kupitia Kampuni ya Sotta Minining Corporation Limited, inayomilikiwa kwa ubia na Serikali ya Tanzania.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde kwenye picha na Ujumbe wa Kampuni ya Perseus Mining Limited na Sotta Minining Corporation Limited mara baada ya mazungumzo yao, Ikulu ya Chamwino, Dodoma tarehe 6 Mei, 2026.

Perseus Mining Limited ni mwekezaji wa Mgodi wa Dhahabu wa Nyanzaga, Wilayani Sengerema, Mkoani Mwanza kupitia Kampuni ya Sotta Minining Corporation Limited, inayomilikiwa kwa ubia na Serikali ya Tanzania.








 

Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Serikali imetangaza kuwa ipo katika hatua za mwisho za kuandaa mfumo wa kisheria pamoja na sera maalum zitakazosimamia huduma za upandikizaji wa viungo, ikiwa ni jitihada za kurasimisha na kuimarisha sekta hiyo muhimu ya afya nchini.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kongamano la kimataifa la kisayansi lililoandaliwa na Hospitali ya Benjamin Mkapa lililolenga kujadili sera, mwelekeo na mikakati ya kuendeleza huduma za upandikizaji viungo, Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Grace Magembe, alisema maandalizi hayo yanatarajiwa kukamilika ifikapo Septemba mwaka huu.

Amesema  kuwa uwepo wa sera na sheria hizo utaweka misingi imara ya utoaji huduma hizo kwa kuzingatia viwango vya kitaifa na kimataifa, hali itakayosaidia kuongeza ufanisi na usalama kwa wagonjwa.

Dkt. Magembe alibainisha kuwa Tanzania imepiga hatua kubwa katika utoaji wa huduma za kibingwa na ubingwa bobezi, jambo linalowezesha wagonjwa wengi kupata matibabu ya hali ya juu ndani ya nchi badala ya kusafiri nje ya mipaka.

Alitaja mafanikio hayo kuwa ni pamoja na huduma za upandikizaji wa uloto kwa wagonjwa wa saratani ya damu pamoja na upandikizaji wa figo, huku akieleza kuwa mipango inaendelea ya kuanzisha huduma za upandikizaji wa ini na moyo katika siku za usoni.

Pamoja na mafanikio hayo, Dkt. Magembe alisisitiza umuhimu wa wananchi kujiunga na mifumo ya bima ya afya, akieleza kuwa huduma za upandikizaji viungo zina gharama kubwa ambazo si rahisi kumudu bila bima.

Alifafanua kuwa gharama za upandikizaji wa uloto zinaweza kufikia shilingi milioni 75, huku upandikizaji wa figo ukigharimu takribani shilingi milioni 40, hali inayofanya uwepo wa bima kuwa nguzo muhimu kwa wananchi wengi.

Kwa mujibu wake, hadi sasa zaidi ya wagonjwa 147 wamefanikiwa kufanyiwa upandikizaji wa uloto na figo hapa nchini, hatua inayopunguza utegemezi wa matibabu nje ya nchi na kuokoa gharama kubwa za usafiri na matibabu.

Aidha, alibainisha kuwa wagonjwa wa figo wanaohitaji huduma ya kuchuja damu hulazimika kufanya hivyo mara kadhaa kwa wiki, jambo linaloambatana na gharama na changamoto kubwa za maisha, hivyo bima ya afya inaweza kuwa suluhisho muhimu kwao.

“Ni muhimu wananchi wakaona umuhimu wa bima ya afya kama wanavyochukulia bima ya magari, kwa sababu inasaidia kukabiliana na gharama kubwa za matibabu,” alisisitiza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Benjamini Mkapa, Profesa Abel Makubi, aliipongeza serikali kwa uwekezaji mkubwa katika sekta ya afya, akisema hatua hiyo imewezesha kuboreshwa kwa huduma za kibingwa nchini.

Ameeleza kuwa kongamano hilo limewakutanisha zaidi ya wataalamu 150 wa afya kutoka mataifa mbalimbali kwa lengo la kubadilishana uzoefu na kuimarisha ujuzi katika huduma za kisasa za matibabu.

Profesa Makubi aliongeza kuwa hospitali hiyo imejikita katika kuendeleza huduma za upandikizaji viungo na itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha huduma hizo zinapanuka zaidi.

Kwa upande wa wanufaika, baadhi ya wagonjwa waliopatiwa huduma hizo walieleza mafanikio yao, wakisema matibabu hayo yamebadilisha maisha yao kwa kiwango kikubwa.

Miongoni mwao ni Richard Masimba, aliyefanyiwa upandikizaji wa figo miezi sita iliyopita, ambaye alieleza shukrani zake kwa madaktari na serikali kwa kumpa nafasi ya kuendelea kuishi maisha ya kawaida.

Naye Nasra Gwota alisema kabla ya kupandikizwa uloto alikuwa akisumbuliwa mara kwa mara na kulazimika kukosa masomo, lakini kwa sasa anaendelea vizuri na kurejea katika shughuli zake za kila siku.








 

Mwamvua Mwinyi, Pwani Mei 6, 2026

WATU wawili wamefariki dunia na wengine 14 kujeruhiwa kufuatia mgogoro wa ardhi uliotokea katika eneo la Vikawe (Lupaso), Kata ya Pangani, Wilaya ya Kibaha mkoani Pwani.
Akizungumza Mei 6, 2026, ofisini kwake wakati wa mkutano na waandishi wa habari, Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Mkoa wa Pwani, ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa huo, Abubakar Kunenge amekiri kutokea tukio hilo la uvunjifu wa amani . 

Amesema watu wasiojulikana walifika katika eneo hilo wakidaiwa kuwa na lengo la kuwaondoa wakazi wanaodaiwa kuvamia ardhi inayomilikiwa kihalali, hali iliyosababisha vifo vya watu wawili . 

Kunenge alieleza kuwa majeruhi wote wanapatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Pwani (Tumbi), huku miili ya marehemu ikiwa imehifadhiwa katika hospitali hiyo.

Jeshi la Polisi mkoani humo linaendelea na uchunguzi ili kubaini chanzo cha tukio hilo, mmiliki halali wa eneo pamoja na waliowatuma watu hao kwenda kuwaondoa wakazi.

Vilevile, amewataka wananchi kujiepusha na kujichukulia sheria mkononi  na uvamizi wa maeneo yasiyo yao.

“Wamiliki wa ardhi wanapaswa kufuata taratibu za kisheria wanapokumbana na migogoro, ikiwemo kufikisha suala hilo katika mabaraza ya ardhi au mahakamani. 

Pia,wamiliki endapo kuna amri ya mahakama ya kubomoa nyumba, washirikishe vyombo vya dola badala ya kuchukua hatua binafsi,” amesisitiza Kunenge.

Kwa upande wake, mkazi wa Chato, Vikawe, Kidawa Hamidu, aliiomba Serikali ya Mkoa pamoja na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuingilia kati mgogoro huo ili haki ipatikane kwa pande zote.

Naye Mwenyekiti wa Vikawe Shule, Shaban Shaban, alisema mgogoro huo ulikuwepo muda mrefu na tayari vikao mbalimbali vilishafanyika kutafuta suluhu, lakini bado haijafahamika nani aliwatuma watu hao kwenda kuwaondoa wananchi.

"Coaster zilikuwa kama tano, wakiwemo watu zaidi ya 200 wakidai wametumwa kwenda kubomoa nyumba za watu waliovamia eneo hilo" 

Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Dharura kutoka Hospitali ya Rufaa ya Tumbi, Siaely Moshi, alithibitisha kupokea majeruhi hao sanjali na vifo vya watu wawili wanaume, akieleza kuwa majeruhi kumi wanaendelea kupatiwa matibabu na wengine wanaendelea vizuri. 




 

 


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Dkt. Evaline Wilbard Munisi kuwa Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi Ajira na Mahusiano) kwenye hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma, tarehe 06 Mei, 2026.
Viongozi mbalimbali wakiapa kiapo cha Maadili kwenye hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 06 Mei, 2026. Kutoka kulia ni; Ndugu Kheri Abdul Mahimbali Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), Balozi Ali Jabir Mwadini, Katibu wa Rais, Mhandisi Peter Phillip Mwasalyanda Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Dkt. Jabir Kuwe Bakari Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Mhe. Angela Charles Kizigha, Mshauri wa Rais, Masuala ya Jamii




Viongozi mbalimbali wakiwa kwenye hafla ya Uapisho wa Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi Ajira na Mahusiano) Mhe. Dkt. Evaline Wilbard Munisi, Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 06 Mei, 2026


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Viongozi mbalimbali mara baada ya kumuapisha Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi Ajira na Mahusiano) Mhe. Dkt. Evaline Wilbard Munisi, Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 06 Mei, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na Waziri Mkuu Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, Spika wa Bunge Mhe. Mussa Azzan Zungu, Katibu Mkuu Kiongozi Mhe. Balozi Dkt. Moses Kusiluka, Kamishna wa Maadili Mhe. Jaji Sivangilwa Mwangesi katika picha na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi Ajira na Mahusiano) Dkt. Evaline Wilbard Munisi, Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 06 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi Ajira na Mahusiano) Dkt. Evaline Wilbard Munisi, Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 06 Mei, 2026.

WANANCHI wa manispaa ya Moshi mkoani Kilimanjaro wamelalamikia gharama za nauli za bajaji zinazofanya ruti zake kama daladala ndani ya manispaa hiyo na kuiomba Serikali kuingilia kati kunusuru adha hiyo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wananchi hao wamedai kuwa hapo awali walikuwa wakitozwa nauli ya 700 lakini kwa sasa wanatozwa 1,000- 1500 hali ambayo imegeuka kuwa adha kwao na kuwafanya wengi kushindwa kumudu gharama

Mmoja wa wananchi hao, Amina Salimu mkazi wa Soweto amesema kuwa, kwa sasa wamekuwa wakilazimika kutembea kwa miguu kutoka mjini Moshi kwenda na kurudi Soweto kutokana na kushindwa kuimili gharama za nauli.

"Mwanzoni tulikuwa tunatumia 1400 kwenda na kurudi Soweto lakini kwa sasa imeongezeka mpaka kufikia 2,000 hadi 3000 hii ni gharama ya kutuumiza sisi wananchi tunaiomba serikali kuingilia kati kutunusuru wananchi" alisema Amina.

Naye Rukia Juma ambaye ni mama lishe na mkazi wa Msaranga alisema kuwa kwa sasa ameanza kushindwa kumudu gharama za kuendesha familia kwani amekuwa akilipwa 4000 kwa siku lakini analazimika kutumia 3000 kwa ajili ya nauli hali ambayo imelekea kushindwa kumudu kutunza familia.

Mwananchi mwingine, Christofa Lyimo alisema kuwa, kwa sasa wamekuwa wakishindwa kwenda hospitali ya KCMC kuwaangalia na kuwahudumia wagonjwa wao ambao wamelazwa katika hospitali hiyo kutokana na gharama za usafiri kupanda.

Akijibu malalamiko hayo, Meneja wa mamlaka ya uthibiti wa usafiri ardhini (LATRA)mkoa wa Kilimanjaro, Paul Nyello alisema kuwa, Sheria ya LATRA haifanyi udhibiti wa tozo za bajaji na ni makubaliano ya abiria na mtoa huduma.

Alisema kuwa kwa sasa wapo katika mchakato wa kuongeza mabasi njia za mjini.


 



Na: Jawadu Kinyobwa – Arusha

Serikali imeagiza waajiri na wasimamizi wa rasilimaliwatu nchini kuhakikisha watumishi wote wenye sifa na waliotengewa bajeti ya kupandishwa Vvyeo Mei mwaka huu wanapandishwa vyeo bila kuwapo kwa ucheleweshaji wowote. 

Agizo hilo linasisitiza kukamilika kwa taratibu zote za kisheria na kanuni kwa wakati, huku Serikali ikionya kuwa haitavumilia malalamiko ya watumishi ambao haki zao zinakwama kutokana na uzembe wa maafisa utawala.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete, ametoa msimamo huo wakati akifungua mkutano wa pili wa Jumuiya za Wataalamu wa Utawala na Rasilimaliwatu (AAPAM Tawi la Tanzania) jijini Arusha Mei 06, 2026.

 Amebainisha kuwa Ofisi yake haitegemei kupokea malalamiko ya watumishi walioachwa wenye sifa huku akisisitiza kuwa watumishi waliojiendeleza lazima wabadilishiwe kada kulingana na miongozo iliyowekwa, kwani kufanya kinyume ni kutowajibika ipasavyo.

Waziri Kikwete ameeleza kuwa mageuzi ya utumishi wa umma yanategemea kwa kiasi kikubwa mchango wa wataalamu hao wa utawala na rasilimaliwatu.

Katika hatua nyingine, Waziri Kikwete ameagiza mabadiliko makubwa ya utendaji kazi ndani ya utumishi wa umma, akisisitiza kuwa kuanzia sasa maafisa rasilimaliwatu na utawala nchini lazima wahakikishe wanajenga usalama wa kisaikolojia kwa watumishi. 

Aidha Waziri amebainisha kuwa viongozi hao wana wajibu wa kutengeneza mazingira yanayofikika ili watumishi waweze kueleza changamoto zao bila hofu, hatua itakayosaidia kuepuka msongo wa mawazo na kuimarisha afya ya akili maeneo ya kazi.

Katika msisitizo wa matumizi ya teknolojia, Waziri ameelekeza matumizi kamili ya mifumo ya kielektroniki ikiwemo e-uhamisho, ambapo amepiga marufuku matumizi ya barua za kawaida katika mchakato wa uhamisho wa watumishi. 
Waziri amesisitiza pia umuhimu wa kuzingatia mwongozo wa kujitolea katika utumishi wa umma wa mwaka 2025, akitaka fursa za vijana kutolewa kwa njia ya uwazi na haki bila upendeleo wowote.

 Aidha, amewataka maafisa hao kuwa viongozi wa mageuzi katika taasisi zao kwa kupunguza urasimu na kushughulikia kero za watumishi katika ngazi ya taasisi badala ya kuziacha kuwa mzigo kwa mamlaka za juu. wananchi.

Vilevile, amewaagiza wataalamu hao kuhakikisha wanazingatia uadilifu na uzalendo kwa kuepuka matumizi ya lugha zisizofaa wanapowahudumia wateja wao, jambo ambalo linaharibu taswira ya serikali. 

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo, Xavier Daudi, amesema serikali imefanya maboresho ya muundo wa maofisa rasilimali watu tangu Septemba mwaka jana, ikiwa ni pamoja na kuhuisha mitaala na kuanzisha bodi ya kitaaluma kwa maofisa hao ili kuimarisha maadili na utendaji wao.

Naye Mwenyekiti wa AAPAM tawi la Tanzania, Leila Mavika, amesema zaidi ya washiriki 1,300 wamehudhuria mkutano huo, akibainisha kuwa unatoa fursa ya kubadilishana uzoefu na kujadili changamoto za kiutendaji katika sekta ya rasilimali watu.

Kwa upande wake, Rais wa AAPAM Afrika, Dk,John Nakabago, alisisitiza umuhimu wa serikali kuwekeza katika miundombinu ya kidijitali na kuhakikisha upatikanaji wa teknolojia kwa wote ili kufanikisha mageuzi ya kidijitali

Aliongeza kuwa ni muhimu kuwajengea uwezo watumishi wa umma, hususan walioko vijijini, ili waweze kutumia teknolojia ipasavyo. Pia alihimiza ushirikiano kati ya serikali, sekta binafsi, vyuo vikuu na asasi za kiraia katika kukabiliana na changamoto za ajira kwa vijana na mazingira.




 

Waziri Mkuu Mstaafu, Kassimu Majaliwa (katikati) akipiga makofi baada ya kuzindua mpango wa uuzaji wa hisa stahiki wa Benki ya Biashara ya Mwalimu ikilenga kuongeza mtaji wa benki, kuongeza uwekezaji na kuimarisha utoaji wa mikopo nafuu kwa walimu na wafanyabiashara wadogo. Hafla hiyo imefanyika leo Mei 6, 2026 Jijini Dar es Salaam


Na Karama Kenyunko, Michuzi TV
WAZIRI Mkuu Mstaafu, Kassimu Majaliwa amezindua mpango wa uuzaji wa hisa stahiki wa Mwalimu Commercial Bank (MCB), ukilenga kuongeza mtaji, uwekezaji na kuimarisha utoaji wa mikopo nafuu kwa walimu na wafanyabiashara wadogo.

Akizungumza Dar es Salaam leo Mei 5, 2026 wakati wa uzinduzi wa mpango huo, Majaliwa amesema uzinduzi wa hisa stahiki unatoa fursa kwa wanahisa wote, akiwemo yeye mwenyewe, kuongeza umiliki katika benki hiyo.

Ameeleza kupitia mpango huo, benki hiyo itaongeza mtaji wake ili kupanua huduma kwa wananchi wengi zaidi, kuimarisha utoaji wa mikopo na kuendeleza teknolojia za kidigitali na kuongeza ushirikishwaji wa kifedha nchini.

Amesema hisa stahiki itaongeza thamani ya uwekezaji wao kama wanahisa na kwamba si fursa ya kifedha pekee, bali fursa ya kuchangia ukuaji wa benki hiyo na kuchangia katika maendeleo ya uchumi wa taifa.

"Nitoe mwito kwa wanahisa wote wa MCB tusikae pembeni. Huu ni wakati wetu wa kuonyesha imani yetu kwa benki yetu na tuchukue hatua ya kununua hisa hizi stahiki, si kwa sababu ya faida pekee, bali kwa sababu tunatambua tunajenga urithi wa kifedha kwa vizazi vijavyo," amefafanua.

Aidha, Majaliwa ameipongeza bodi na uongozi kwa busara na dira thabiti inayoweka benki hiyo katika njia sahihi ya ukuaji na kuwataka kuendelea na kasi hii ya ubunifu, uwazi na utumishi bora kwa wateja.

Naye, Mwenyekiti wa bodi ya MCB, Francis Ramadhani amesema katika zoezi la Hisa Stahiki, wanahisa wote ambao majina yao yapo kwenye rejesta ya wanahisa kufikia Mei 5, 2026, wana haki ya kununua hisa mpya tatu kwa kila hisa moja waliyonayo.

Amefafanua hisa hizo zitauzwa kwa bei ya punguzo ya Sh 110 na dirisha la ununuzi wa hisa stahiki limefunguliwa na wanahisa wataweza kununua hisa za benki kidigitali kupitia Soko la hisa la Dar es Salaam (DSE) Hisa Kiganjani, Ofisi za Chama cha Walimu (CWT) na matawi na ofisi za benki ya Mwalimu.

"Hisa Stahiki ni fursa ya kipekee kwa wanahisa wa benki kununua hisa za ziada kwa bei ya punguzo kabla zoezi kufungwa. Hatua hii ni muhimu sana kwani inalenga kuimarisha mtaji wa benki, kuwezesha ukuaji endelevu wa biashara na kuboresha huduma tunazotoa kwa wateja wetu kote nchini," amesema

Amesisitiza mpango huo umepata idhini kutoka Benki Kuu (BOT) na litafanyika kwa uwazi chini ya usimamizi CMSA, DSE kwa ushirikiano na iTrust Finance Limited ambao ni washauri wao.

"Tunawahimiza wanahisa kushiriki, ili kuhakikisha kuwa benki yetu inapata mtaji wa ziada utakaosaidia kutanua wigo wa mikopo, kuimarisha huduma za kidijitali na kutimiza viwango vya kisheria vya mtaji vilivyowekwa na BOT," amesema.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa benki hiyo, Richard Makungwa amesema katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, benki hiyo imefanikiwa kuongeza mali kutoka chini ya Sh bilioni 30 mwaka 2019 hadi Sh bilioni 98 mwaka jana, ukuaji unaoakisi ufanisi wa usimamizi wa rasilimali na kuongezeka kwa shughuli za kibenki.

Pia amana za wateja zimeongezeka kutoka wastani wa Sh bilioni 16 hadi zaidi ya Sh bilioni 75 (2025), ikionesha imani kubwa ya wateja na wanahisa kwa benki.

"Mikopo imeongezeka kutoka Sh bilioni 16 (2019) hadi Sh bilioni 66 (2025), tukilenga wateja binafsi hususani walimu, watumishi wengine, wafanya biashara wadogo na kati (SME) ambao ni nguzo za uchumi wa Taifa," amesema.

Kadhalika, faida kabla ya kodi imeongezeka kutoka hasara ya Sh bilioni 4.8 (2019) hadi faida ya Sh milioni 487 (2025), ikiashiria mwenendo chanya wa kibiashara na usimamizi bora wa gharama.

Madhumuni ya benki hiyo ni kuongoza katika ubunifu wa huduma za kifedha, kuongeza thamani, uadilifu na uwajibikaji kwa kijamii.

"Tunajipanga kuona ukuaji endelevu wa faida kwa wanahisa wetu, kuimarika kwa huduma za kidigitali ili kuongeza ujumuishi wa kifedha na kuendelea kutoa mchango mkubwa kwa maendeleo ya taifa kupitia uwezeshaji wa elimu, vijana na sekta ya uzalishaji," amesisitiza.
Waziri Mkuu Mstaafu, Kassimu Majaliwa akizungumza wakati wa uzinduzi wa mpango wa uuzaji wa hisa stahiki wa Benki ya Biashara ya Mwalimu ikilenga kuongeza mtaji wa benki, kuongeza uwekezaji na kuimarisha utoaji wa mikopo nafuu kwa walimu na wafanyabiashara wadogo. Hafla hiyo imefanyika leo Mei 6, 2026 Jijini Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa Bodi ya MCB, Francis Ramadhani akizungumza wakati wa uzinduzi wa mpango wa uuzaji wa hisa stahiki wa Benki ya Biashara ya Mwalimu ikilenga kuongeza mtaji wa benki, kuongeza uwekezaji na kuimarisha utoaji wa mikopo nafuu kwa walimu na wafanyabiashara wadogo. Hafla hiyo imefanyika leo Mei 6, 2026 Jijini Dar es Salaam.






Mei 5, 2026,
KAMPUNI ya Airtel Tanzania na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) wameingia makubaliano ya kimkakati ya miaka mitatu ya kuimarisha na kupanua jukwaa la mafunzo ya ufundi linalotegemea simu za mkononi, likilenga kuongeza upatikanaji wa elimu ya ujuzi kwa Watanzania kote nchini.

Makubaliano hayo yanaifanya Airtel VSOMO kuwa jukwaa rasmi la taifa la mafunzo ya ufundi stadi mtandaoni chini ya VETA.

Chini ya ushirikiano huo mpya, Airtel Tanzania itaendelea kutoa msaada wa kina kupitia miundombinu ya mawasiliano ya nchi nzima, teknolojia ya kidigitali, huduma ya matumizi bila gharama ya data (zero-rated access), pamoja na kampeni za uhamasishaji zinazolenga kuongeza kasi ya matumizi ya elimu ya kidigitali nchini.

Akizungumza wakati wa hafla ya utiaji saini, Mkurugenzi Mtendaji wa Airtel Tanzania, Charles Kamoto, alisema ushirikiano huo unaonesha dhamira ya Airtel katika kuendeleza mageuzi jumuishi ya kidigitali na kupanua upatikanaji wa elimu ya ujuzi kwa Watanzania.

“Airtel VSOMO ni jukwaa rasmi la taifa la mafunzo ya ufundi stadi mtandaoni chini ya VETA. Linawawezesha Watanzania kupata ujuzi wa vitendo wakati wowote na mahali popote kupitia vifaa vyao vya kidigitali,” alisema Kamoto.

Alisisitiza kuwa mchango wa Airtel hauishii kwenye mawasiliano pekee, bali unajumuisha uwekezaji mpana katika ujumuishaji wa kidigitali, elimu na uwezeshaji wa vijana.

“Sisi Airtel hatujihusishi tu na kutoa huduma ya mtandao. Tunahamasisha kikamilifu matumizi ya Airtel VSOMO, tunatoa huduma ya bila gharama ya data, na kuhakikisha gharama si kikwazo kwa Watanzania kujifunza na kujiendeleza,” aliongeza.

Kamoto alibainisha kuwa mfumo wa kidigitali wa Airtel unaendelea kuendesha jukwaa hilo kupitia mtandao mpana wa nchi nzima, huduma imara za data na miundombinu ya fedha kupitia simu, inayowezesha watumiaji kujisajili, kulipia kozi na kupata maudhui ya mafunzo kwa urahisi.

Aliongeza kuwa Airtel ina zaidi ya wateja milioni 23.7 wanaotumia huduma zake, akisema mtandao huo unaiwezesha Airtel VSOMO kuwafikia wanafunzi mijini na vijijini. Pia alieleza kuwa huduma ya matumizi ya bure ya data imepunguza kwa kiasi kikubwa gharama za elimu ya mtandaoni kwa maelfu ya watumiaji.

Takwimu za Airtel zinaonesha kuwa Airtel VSOMO imepakuliwa mara 59,000, ambapo takribani asilimia 60 ya matumizi yamefanyika kupitia huduma ya bure ya data ya Airtel. Jumla ya watumiaji 27,194 wamejisajili kwenye jukwaa hilo, huku wanafunzi 9,539 wakijiunga na programu mbalimbali za ufundi stadi.

Kati ya hao, wanafunzi 6,723 tayari wamehitimu mafunzo yao, jambo linaloonesha ongezeko la matumizi na mafanikio katika elimu ya ufundi stadi ya kidigitali.

Airtel pia imewekeza tena takribani TZS milioni 80.6 kutoka katika sehemu ya ada za mafunzo kurudi VETA ili kusaidia upanuzi wa jukwaa, uandaaji wa maudhui na uimarishaji wa mifumo. Aidha, Airtel VSOMO imezalisha thamani ya kiuchumi inayokadiriwa kufikia TZS bilioni 1.2, huku wanafunzi wakihifadhi wastani wa TZS 180,000 kila mmoja ikilinganishwa na njia za kawaida za mafunzo.

Jukwaa la Airtel VSOMO pia limeunganishwa na mfumo wa Fundi Connect, unaowawezesha wahitimu wa VETA kusajili ujuzi wao na kuunganishwa moja kwa moja na wateja, hivyo kuimarisha uhusiano kati ya mafunzo na ajira pamoja na kusaidia ujasiriamali wa vijana.

Airtel VSOMO pia inalingana na mradi wa East Africa Skills for Transformation and Regional Integration Project (EASTRIP), unaolenga kutambua na kusawazisha vyeti vya ufundi stadi kati ya Tanzania, Kenya na Ethiopia, hatua inayoongeza uhamaji wa wafanyakazi na fursa za ajira kikanda.

Ushirikiano huo unaunga mkono ajenda ya maendeleo ya taifa chini ya Dira ya Maendeleo 2030, na kuimarisha juhudi za serikali za kuongeza ajira kwa vijana chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.

Mkurugenzi Mkuu wa VETA alitoa shukrani kwa Airtel Tanzania kwa kuendelea kusaidia maendeleo ya elimu ya ufundi kupitia mageuzi ya kidigitali.

“Tunaishukuru sana Airtel Tanzania kwa msaada wao endelevu, hasa katika kutoa huduma ya intaneti na kuwezesha upatikanaji mpana wa Airtel VSOMO. Ushirikiano huu umetuwezesha kuwafikia vijana wengi zaidi kuliko hapo awali,” alisema.

Alibainisha kuwa ushirikiano huo umeongeza kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa mafunzo na kuboresha unyumbufu wa utoaji wa elimu nchini.

Aliongeza kuwa Airtel VSOMO sasa ni mfumo rasmi wa kidigitali wa mafunzo ya ufundi stadi chini ya VETA, unaokamilisha vituo vya mafunzo vya kawaida na kupanua wigo wa kitaifa.

Pia alieleza kuwa awali VETA ilikuwa inapokea maombi takribani 12,000 kwa mwaka, lakini uwezo wake ulikuwa unaruhusu kuchukua wanafunzi 3,000 pekee kutokana na vikwazo vya miundombinu ya vituo vya mafunzo.

“Kupitia Airtel VSOMO, tunapanua wigo ili vijana wengi zaidi wapate ujuzi wa vitendo kwa ajili ya ajira na kujiajiri popote walipo,” alisema.

Taasisizo hizo mbili zimeweka lengo la pamoja la kuandikisha angalau wanafunzi 400 wapya kila mwezi kupitia Airtel VSOMO, kama sehemu ya kuendelea kupanua elimu ya ujuzi wa kidigitali na kuimarisha ajira kwa vijana nchini Tanzania.


Top News