Na Mwandishi Wetu
WAZIRI wa zamani wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka amewataka wakaguzi wa shule kutenda haki kwa shule binafsi na kuziona kama mshirika wa maendeleo badala ya mshindani.

Kadhalika, Profesa Tibaijuka ameipongeza shule ya St Anne Marie Academy kwa kuendelea kusomesha bure wanafunzi wanaofiwa na wazazi wao ikiwa shule pekee ya binafsi inayofanya hivyo kwa sasa nchini.

Alitoa pongezi hizo mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam wakati wa maadhimisho ya miaka 25 ya kuanzishwa kwa shule hiyo Julai 18, mwaka 2001.

Aliwataka wakaguzi wa elimu nchini kuacha kuziwekea vikwazo shule binafsi kwa kuziona kama washindani kwenye sekta ya elimu na badala yake wanatakiwa kuwaona kama washirika muhimu kwenye kutoa huduma hiyo.

”Unakuta wanawawekea wenye shule binafsi viwango vya kusadikika tofauti kabisa na shule za umma, sisemi kwama muwawekee viwango hafifu, hapana mimi nataka uwiano wa haki baina ya shule za umma na shule binafsi,” alisema

Alisema shule zingine zinapaswa kuiga mfano huo kwani elimu ni huduma na siyo biashara hivyo wanatakiwa kuwaacha waendelee na masomo baada ya wazazi wao wanaowalipia ada kufariki dunia.

Kadhalika, Profesa Tibaijuka alisema serikali imebadili mitaala ya zamani na kuingiza mitaala ya ufundi ambayo inamwezesha mwanafunzi kuchagua na hivyo kupata ujuzi utakaowawezesha kupata ajira au kujiajiri mapema wanapomaliza masomo yao.

Alisema wakati huu wa teknolojia ya kisasa shule zinapaswa kwenda na wakati kwa kuhakikisha zinakwenda sanjari na dunia ya sasa kwa kuwa na mafunzo ya teknolojia ya habari na mawasiliano TEHAMA.

Alisema shule bora ni ile yenye uwezo wa kufaulisha mwanafunzi ambaye alikuwa na matokeo ya kawaida kwani kuna baadhi ya shule ambazo zimekuwa zikichuja wanafunzi na kuchukua wale waliofaulu vizuri pekee.

“Kama mwanafunzi amefaulu kwa daraja la kwanza ili tujue hiyo ni shule bora lazima tujue aliingia akiwa na daraja la ngapi, kuna wanafunzi wengine kwa uwezo wao mkubwa hawahitaji hata mwalimu sasa ukichukua mwanafunzi bora akafaulu huwezi kujisifu,” alisema

“Nawapongeza St Anne Marie Academy kwani wao wamekuwa wakichukua wanafunzi wa kawaida na kuwatengeneza kufaulu kwa wastani wa daraja la kwanza na daraja la pili, nimemsikia Mkurugenzi akitaja mafanikio ya shule imekuwa ikiingiza wanafunzi bora kitaifa kila mwaka nawapongeza sana,” alisema

Mkurugenzi wa shule hiyo, Dkt. Jasson Rweikiza shule hiyo iliwahi kupata mwanafunzi bora kitaifa kwenye somo la hisabati kidato cha nne mwaka 2013, shule hiyo iliingia 10 bora kitaifa kwa miaka mine mfululizo na kwamba mwaka 2021 shule hiyo ilipata mwanafunzi bora kitaifa kwenye masomo yote.


Na Karama Kenyunko Michuzi Tv
SERIKALI imesema itaendelea kuimarisha huduma za afya ya uzazi nchini ili kupunguza vifo vya kina mama vinavyotokana na utoaji mimba usio salama.

Naibu Waziri wa Afya, Dk Florence Samizi alisema bungeni kuwa asilimia 10 ya vifo vya wajawazito nchini vinahusishwa na utoaji mimba usio salama, hali inayoonyesha umuhimu wa kuendelea kuwekeza katika kinga, elimu na huduma za matibabu kwa wanawake.

Alisema Serikali chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan imeboresha miundombinu ya sekta ya afya na kuendelea kutoa huduma jumuishi baada ya utoaji mimba (CPAC) bila malipo katika vituo vya kutolea huduma za afya.

"Tunawapatia wanawake huduma baada ya kuharibikiwa na mimba, ikiwemo matibabu, dawa, ushauri nasaha na elimu ya uzazi wa mpango ili kupunguza hatari ya kupata mimba nyingine isiyotarajiwa na kuzuia madhara yanayoweza kujitokeza," alisema Dk Samizi.

Aliongeza kuwa serikali inaendelea kuimarisha huduma rafiki kwa vijana kwa kutoa elimu ya afya ya uzazi, kujikinga dhidi ya mimba zisizotarajiwa na maambukizi ya magonjwa, pamoja na kuhakikisha manusura wa ukatili wa kijinsia na matukio mengine wanapata huduma stahiki kwa wakati.

Kauli hiyo imekuja wakati wadau mbalimbali wakiendelea kujadili utekelezaji wa Itifaki ya Maputo, ambayo Tanzania iliiridhia.

Mjadala umejikita zaidi kwenye Ibara ya 14(2)(c) ya itifaki hiyo, inayozitaka nchi wanachama kuchukua hatua zinazofaa kuruhusu utoaji mimba kwa njia ya tiba katika mazingira maalumu, ikiwemo pale ujauzito umetokana na ubakaji, unyanyasaji wa kingono, ndugu wa damu (incest), au endapo kuendelea kwa ujauzito kunaweka maisha au afya ya mama katika hatari, au maisha ya kijusi yako hatarini. Utekelezaji wa masharti hayo unafanyika kwa kuzingatia sheria za ndani za kila nchi.

Nchini Tanzania, utoaji mimba kwa hiari bado unadhibitiwa na sheria, isipokuwa katika mazingira yanayotambuliwa na sheria husika.

Hata hivyo, Serikali imeendelea kusisitiza kuwa wanawake wanaopata madhara baada ya utoaji mimba wanapaswa kufika katika vituo vya afya ili wapate matibabu, ushauri nasaha na huduma nyingine muhimu bila kuchelewa.

Wataalamu wa afya wanasema utoaji wa huduma hizo, sambamba na elimu ya afya ya uzazi na upatikanaji wa huduma kwa wakati, ni miongoni mwa hatua muhimu zinazoweza kupunguza vifo vya kina mama na kuboresha afya ya uzazi nchini.
Na Mwandishi Wetu
WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, ambaye pia ni Mbunge wa Arusha, Paul Makonda, ameridhishwa na maboresho yanayoendelea katika Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Center inayotoa huduma kwa ushirikiano na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete, ALMC–JKCI Arusha.

Maboresho hayo yanafanyika kwa uwezeshaji wa Global Medicare, kwa lengo la kuongeza ubora wa huduma za afya, kuboresha mazingira ya matibabu, kuimarisha utalii tiba na kuiandaa hospitali kutoa huduma zinazokidhi viwango vya kimataifa kuelekea mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika, AFCON 2027.

“Lengo kubwa ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora kabisa na katika mazingira mazuri. Vilevile tunataka kuimarisha utalii tiba na kutengeneza mazingira mazuri kwa ajili ya AFCON 2027,” alisema Makonda.

Makonda pia alimshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuwekeza katika sekta ya afya na kuruhusu taasisi za kibingwa kama JKCI kupanua huduma zake hadi mikoani.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa JKCI ambaye pia ni Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo, Dkt. Peter Kisenge, alisema maboresho yanayoendelea yanalenga kuibadilisha ALMC–JKCI kuwa kituo cha kisasa cha huduma za kibingwa chenye mazingira rafiki kwa wagonjwa.

Dkt. Kisenge alisema lengo ni kuhakikisha mgonjwa anapofika hospitalini anakutana na mazingira yenye usafi, utulivu, faraja na huduma zinazofanana na zinazopatikana katika hospitali kubwa za kimataifa.

“Tunataka mgonjwa anapokuja hapa asiingie katika mazingira yanayomwongezea hofu. Tunataka akute hospitali yenye mazingira mazuri, tulivu na yenye huduma zinazompa faraja,” alisema Dkt. Kisenge.

Kwa mujibu wake, skrini moja itaonyesha taarifa za wagonjwa waliopo wodini, ikiwemo mapigo ya moyo, kiwango cha oksijeni kwenye damu, shinikizo la damu na viashiria vingine muhimu vya afya.

Skrini nyingine itaunganishwa na mfumo wa Dozee, teknolojia inayowezesha mgonjwa kuendelea kufuatiliwa hata baada ya kuruhusiwa kutoka hospitalini.

Alisema mgonjwa aliyefanyiwa upasuaji, upasuaji wa kujifungua au matibabu mengine yanayohitaji uangalizi wa siku kadhaa ataweza kufuatiliwa akiwa nyumbani, huku wauguzi na madaktari wakipokea taarifa za afya yake kwa wakati.

Dkt. Kisenge alisema mfumo huo utasaidia kugundua mapema mabadiliko ya hali ya mgonjwa na kuwawezesha wataalamu wa afya kuchukua hatua kabla hali haijawa mbaya.

Alisema vyumba vya wagonjwa vitawekewa vifaa vya kisasa vya ufuatiliaji, televisheni na mifumo ya kidijitali ya kuhifadhi historia ya mgonjwa, uchunguzi, dawa na matibabu yote anayopatiwa.

Dkt. Kisenge alisema hospitali pia inaandaa wodi maalumu ya wagonjwa wanaohitaji uangalizi wa karibu baada ya kutoka katika chumba cha wagonjwa mahututi, inayojulikana kama High Dependency Unit.

Dkt. Kisenge alisema mashine ya Cath Lab yenye thamani ya takribani shilingi bilioni tatu inatarajiwa kuwekwa katika hospitali hiyo kwa ajili ya uchunguzi na matibabu ya matatizo ya mishipa ya moyo.

Mkurugenzi wa Huduma za Kliniki wa ALMC–JKCI Arusha, ambaye pia ni Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo, Dkt. Sakeh Mwishete, alisema uongozi wa hospitali umeweka mkakati wa kuhakikisha wagonjwa wenye mahitaji tofauti wanapata huduma zinazowafaa.

Dkt. Mwishete alieleza kuwa vyumba vya VIP vimewekewa vifaa vinavyowezesha kubadilishwa haraka kuwa vyumba vya uangalizi maalumu au ICU endapo hali ya mgonjwa itabadilika.

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Arusha Mji

“Hiki ni chumba cha VIP, lakini kimewekewa vifaa maalumu. Endapo hali ya mgonjwa itabadilika, kinaweza kupandishwa hadhi na kutoa huduma za dharura au huduma zinazohitajika katika ICU bila kuchelewa,” alisema Dkt. Mwishete.

Naye, Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Dharura katika ALMC–JKCI Arusha, Dkt. Farida Abdallah, alisema kitengo cha dharura kinaendelea kupokea wagonjwa kutoka Arusha, Manyara, Singida na maeneo mengine ya Kanda ya Kaskazini.

“Lengo letu kubwa ni kuhakikisha mgonjwa wa dharura anapata huduma kwa wakati ili kuzuia madhara ya kudumu au kupoteza maisha. Mimi pamoja na timu yangu tunafanya kazi saa 24 kuhakikisha wagonjwa wanapata huduma za haraka,” alisema Dkt. Farida.


Serikali kupitia Wizara ya Afya imeendelea kuimarisha utayari wa kukabiliana na ugonjwa wa Ebola kwa kuendesha mafunzo kwa vitendo kwa wataalamu wa afya, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuendelea kuimarisha uwezo wa mfumo wa afya katika kuzuia, kugundua na kutoa mwitikio wa haraka dhidi ya magonjwa ya mlipuko.

Hayo yamesemwa Julai 17,2026, na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Dkt. Ibrahim Isack, wakati wa zoezi la usimamizi shirikishi na mafunzo kwa vitendo ya kukabiliana na magonjwa ya mlipuko, amesema kuwa maandalizi ya kutosha ndiyo msingi wa kudhibiti athari za milipuko kwa wananchi.

“Ebola ni ugonjwa unaohitaji umakini mkubwa na hatua za haraka. Wataalamu wa afya wanapaswa kuwa na uwezo wa kutambua viashiria vya awali, kutoa taarifa kwa wakati na kuanzisha hatua za awali za udhibiti ili kuzuia kusambaa kwa maambukizi,” amesema Dkt. Isack.

Amesema usimamizi shirikisishi na mafunzo kwa vitendo hutoa nafasi ya kutathmini utendaji wa huduma za afya katika mazingira yanayofanana na hali halisi, jambo linalosaidia kubaini mapungufu yaliyopo na kuweka mikakati ya kuyafanyia kazi kabla ya kutokea kwa dharura.

Aidha, Dkt. Isack amesema mafanikio katika kukabiliana na magonjwa ya mlipuko yanategemea ushirikiano wa karibu kati ya wataalamu wa afya, viongozi wa sekta ya afya na taasisi mbalimbali, ili kuhakikisha kila ngazi inatimiza wajibu wake kwa wakati na kwa ufanisi.

Kwa upande wake, Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Dharura kutoka wizara ya afya, Dkt. Michael Kiremeji amesema mafunzo hayo yanalenga kuendelea kujenga umahiri wa wataalamu wa afya katika kutoa huduma salama na kufuata taratibu za kitaalamu wakati wa kukabiliana na magonjwa ya mlipuko, hatua inayochangia kuimarisha usalama wa wagonjwa na wahudumu wa afya.

Ameongeza kuwa Wizara ya Afya itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuendesha mafunzo na usimamizi shirikishi katika maeneo mbalimbali nchini, kwa lengo la kuimarisha mfumo wa afya, kuongeza utayari wa kukabiliana na dharura za afya ya umma na kulinda afya za wananchi.









KUTOKA VUNJO

MBUNGE wa Jimbo la Vunjo mkoani Kilimanjaro, Enock amewahimiza vijana kuendelea kumcha Mungu, kuzingatia maadili mema na kujiepusha na vitendo vinavyoweza kuhatarisha maisha na mustakabali wao.

Koola alitoa kauli hiyo leo wakati wa ufunguzi wa bonanza la michezo la vijana wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Jimbo la Kilimanjaro mashariki lililofanyika Marangu mashariki lililowakutanisha vijana 500 kutoka maeneo mbalimbali ya jimbo hilo.

Koola aliwasisitiza vijana kujiepusha na makundi ya kihalifu, kuwa wazalendo na kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo ya jamii na taifa.

Bonanza hilo linalenga kuimarisha umoja, mshikamano na ushirikiano miongoni mwa vijana kupitia ibada, maombi, kujifunza Neno la Mungu na kushiriki michezo mbalimbali inayokuza afya, nidhamu na maendeleo ya kijamii.

Alieleza kuwa, Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Vunjo imeendelea kutekeleza programu mbalimbali zinazolenga kuwawezesha vijana kiuchumi ambapo  zinajumuisha mafunzo ya ufugaji wa kuku wa kibiashara, ufugaji wa ng'ombe wa maziwa, ufugaji wa samaki, kilimo cha kisasa na ujasiriamali, kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kujiajiri na kuongeza kipato.

Alisema kuwa, ofisi yake imewaajiri vijana mahsusi ili kuwasaidia wenzao kuunda vikundi vya kiuchumi, kuandaa katiba za vikundi, kukamilisha nyaraka za maombi ya mikopo ya Halmashauri isiyo na riba, pamoja na kuwaunganisha na taasisi za kifedha zinazotoa mikopo yenye masharti nafuu.

Alisisitiza kuwa uwekezaji kwa vijana ni msingi wa maendeleo endelevu ya Jimbo la Vunjo na Taifa kwa ujumla na kuahidi kuendelea kushirikiana na taasisi za dini na wadau mbalimbali katika kuwawezesha vijana kupata elimu, stadi za maisha na fursa za kiuchumi zitakazowasaidia kujenga maisha bora na kuchangia maendeleo ya nchi.






NA MWANDISHI WETU



DIWANI wa Kata ya Kinondoni, wilayani Kinondoni, mkoani Dar es Salaam, Idrissa Said Ngatiche (CCM), amesema atafanya jitihada kubwa kuhakikisha watu wenye ulemavu katika kata hiyo wananufaika na kuzifikia fursa muhimu hususan ni za kiuchumi.

Ameyasema hayo leo katika mkutano wa Siku ya Watu Wenye Ulemavu Kinondoni, aliyoandaa maalumu kusikiliza na kutatatua kero za kundi hilo, kula chakulacha pamoja na kukabidhi msaada wa viti mwendo viwili.

Ngatiche amesema, kundi hilo ni muhimu kushirikishwa kikamilifu katika shughuli za kiuchumi ikiwemo kunufaika na mikopo ya asilimia 15 inayotolewa na Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni kwa vikundi vya wajasiriamali wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.

"Kutokana na hali hiyo leo nimeandaa Siku Maalumu ya Watu Wenye Ulemavu Kinondoni, kwa nia ya kuwatambua, kujua idadi yao na kuwasikiliza changamoto zao.Kundi hili limekuwa likisahaulika sana, hivyo kama diwani nimetumia jukwaa hili leo kuwakusanya pamoja ili wanufaike na fursa zilizopo kama makundi mengine,"amesema Ngatiche.

Ameeleza huo ni mwanzo wa hatua zake za kulisaidia kundi hilo huku akitoa wito kwa jamii kuto kuwaficha watu wenye ulemavu hususan watoto ambao wanatakiwa kwenda shule.

"Jamii isiwafiche watu wenye ulemavu. Serikali yetu chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, haijawatenga ndiyo maana katika ile mikopo ya asilimia 15 inayotolewa na halmashauri inatenga asilimia mbili kwaajili ya vikundi vya wenye ulemavu,"ameeleza Ngatiche.

Diwani huyo, amekabidhi viti mwendo viwili kwa watu wenye ulemavu wawili ambao ni mtoto Brighton Michael na mtu mzima Daud Anthon.

Mwenyekiti wa Watu wenye Ulemavu hao Ali Maulid Ali, amempongeza Diwani Ngatiche, kwa jitihada zake za kuwatambua na kuwasaidia watu wenye ulemavu kwani kundi hilo limekuwa likisahaulika.

Maulid amesema kundi kundi hilo linanguvu na halipo kinyonge na mutano huo ni chachu ya kuanzisha umoja wenye nguvu wa watu wenye ulemavu.

" Tunamshukuru sana Rais dk. Samia, nchi iko salama. Yakitokea machafuko sisi wenye ulemavu ndiyo waathirika wakubwa, hivyo tuwakemee watu wanao chochea machafuko. Mkutano huu uwe mwanzo wa sisi watu wenye ulemavu kuwa na umoja wenye nguvu. Hivyo tunamshukuru pia Diwani Ngatiche kwa kuliona hili,"alieleza Maulid.







Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Ujumbe Maalum kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) Mhe. Félix Antoine Tshisekedi, uliowasilishwa kwake na Waziri wa Ushirikiano wa Kikanda Mhe. Floribert Anzuluni Isiloketshi, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 19 Julai, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Mjumbe Maalum wa Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) Mhe. Félix Antoine Tshisekedi, ambaye ni Waziri wa Ushirikiano wa Kikanda Mhe. Floribert Anzuluni Isiloketshi, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 19 Julai, 2026.





Na Karama Kenyunko
UTOAJI wa elimu ya afya ya uzazi, huduma za uzazi wa mpango na mafunzo kwa watoa huduma za afya wa serikali katika vituo vya afya umeelezwa kusaidia kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi, vifo vya watoto wachanga, mimba zisizotarajiwa na kuwasaidia wasichana na vijana kufikia ndoto zao katika kipindi cha miaka 37 ya shughuli za MSI Tanzania nchini.
Akizungumza Ijumaa wiki iliyopita katika maadhimisho ya miaka 37 ya MSI Tanzania tangu ilipoanza kutoa huduma nchini mwaka 1989, Mratibu Msaidizi wa Huduma ya Afya ya Uzazi na Mtoto kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI, Agnes Mgaya, alisema miaka hiyo imekuwa na mafanikio makubwa kupitia ushirikiano kati ya MSI Tanzania na Serikali.

"Miaka 37 siyo mchezo, kuna mabonde na milima. Kuna watu wengi wamejifunza kutoka MSI Tanzania. Nawapongeza watumishi wa MSI Tanzania hasa katika eneo la outreach programme (huduma ya M-koba), mmewezesha watu kupata huduma ya uzazi wa mpango, na pia mmeweza kufanya kazi na watoa huduma wa afya serikalini. Manesi shikizi (Embedded Nurses) wameweza kutoa mafunzo na watumishi hawa wamejifunza kutoka kwa manesi hawa wakiwa kazini na sasa wana uwezo wa kutoa huduma muda wowote kwa mteja katika vituo vyao vya afya," alisema.

Alisema afua zinazotekelezwa na MSI Tanzania kwa kushirikiana na Serikali zimechangia kupunguza vifo vya mama na mtoto kwa asilimia 40.

Mgaya alisema mbali na kutoa huduma za afya ya uzazi na uzazi wa mpango, MSI Tanzania imekuwa ikitoa mafunzo kwa watoa huduma wa afya kuhusu namna ya kupanga mipango ya vituo vya afya, hatua ambayo itasaidia kuandaa na kutekeleza mipango inayochangia kuboresha afya ya watu binafsi na jamii, kuweka vipaumbele na kutumia rasilimali zilizopo kwa ufanisi.
---


Kwa upande wake, Mratibu wa Mkoa wa Afya ya Mama na Mtoto Mkoa wa Dar es Salaam, Rehema Panga, aliipongeza MSI Tanzania kwa mchango wake katika kupunguza vifo vya akina mama na watoto pamoja na mimba zisizotarajiwa.

"Pia tunatambua mchango wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Idadi ya Watu (UNFPA) na United Kingdom's Foreign, Commonwealth and Development Office (FCDO). Mchango wenu ni mkubwa sana. Kama Serikali tunawapongeza sana kwa kuunga mkono juhudi za Serikali katika kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi kwa akina mama na mtoto," alisema.

Alisema kwa mujibu wa tafiti, utoaji wa huduma za uzazi wa mpango unapunguza vifo vitokanavyo na uzazi kwa asilimia 40.

Panga pia aliishukuru MSI Tanzania kwa kufika maeneo yasiyofikika kupitia huduma za M-koba, ambapo imeweza kuwafikia vijana kwa elimu pamoja na kuwapa elimu watu wenye ulemavu.
Naye Mkurugenzi wa MSI Tanzania, Patrick Kinemo, alisema shirika hilo linaendelea kushirikiana na Serikali, washirika wa maendeleo na wadau wengine kuhakikisha wanawake na familia wanaendelea kupata huduma bora za afya ya uzazi na afya ya ngono licha ya changamoto za kifedha.

"Leo tunaadhimisha miaka 37 ya uwepo wa MSI nchini Tanzania na mchango wetu katika sekta ya afya, hususan afya ya uzazi na uzazi wa mpango," alisema.

Kinemo alisema kupungua kwa ufadhili kutoka kwa wafadhili kumesababisha changamoto kwa programu za afya, lakini MSI imepanua vyanzo vya ufadhili na kuimarisha ushirikiano wa kimkakati ili kuhakikisha huduma muhimu zinaendelea kutolewa bila kukatizwa.

Alieleza kuwa shirika hilo limeanzisha mfumo endelevu wa ufadhili unaochanganya misaada ya wafadhili na mapato yanayotokana na masoko ya kijamii pamoja na vituo vya afya, ambapo mapato kutoka hospitali na kliniki zinazohudumia wateja wanaolipia huduma pamoja na wenye bima ya afya hutumika kugharamia huduma za bure za afya ya uzazi na uzazi wa mpango kwa jamii zilizo katika mazingira magumu.

Aliongeza kuwa MSI Tanzania pia huuza bidhaa za afya ya uzazi kama kondomu, njia za uzazi wa mpango na vidonge vya dharura vya uzazi wa mpango, huku mapato hayo yakisaidia programu za huduma za M-koba katika maeneo ya vijijini na maeneo magumu kufikika.
Mwenyekiti wa Bodi ya MSI Tanzania, Magreth Ngasani, alisema ushirikiano wa shirika hilo na Serikali umechangia kuboresha afya ya mama na mtoto kwa kuunga mkono juhudi za kitaifa za kupunguza vifo vya akina mama vinavyoweza kuzuilika.

Alisema uzazi wa mpango unabaki kuwa moja ya hatua muhimu zaidi katika kupunguza vifo vya akina mama kwa kuwa unawawezesha wanawake kupanga na kutenganisha mimba kwa usalama huku ukipunguza hatari za kiafya.

Ngasani alisema mbali na utoaji wa huduma, MSI imekuwa ikiunga mkono programu za Serikali za huduma za M-koba kwa kutoa usafiri, rasilimali za kifedha na msaada wa vifaa unaowawezesha wahudumu wa afya kuwafikia wananchi katika maeneo yasiyofikiwa kwa urahisi.

Aliongeza kuwa shirika hilo pia limewekeza katika kuimarisha mifumo ya afya kwa kuwajengea uwezo wahudumu wa afya katika mipango na usimamizi pamoja na kusaidia vituo vya afya kuandaa mipango bora ya uendeshaji ya kila mwaka na kuboresha utoaji wa huduma.
Kwa upande wake, mwakilishi wa Ofisi ya Uingereza ya Masuala ya Nje, Jumuiya ya Madola na Maendeleo (FCDO), Getrude Mapunda, aliipongeza MSI Tanzania kwa kubadili maisha ya wanawake, wasichana na jamii kupitia utoaji wa huduma za afya ya uzazi, hususan katika maeneo magumu kufikika nchini.

Alisema mafanikio yaliyopatikana katika kuendeleza haki za wanawake na huduma za afya ya uzazi katika kipindi cha miaka 20 iliyopita yanakabiliwa na shinikizo kutokana na mabadiliko ya mazingira ya kisiasa na kijamii, hivyo kuendelea kuwekeza na kuimarisha ushirikiano ni muhimu zaidi kuliko wakati mwingine wowote.

Akikumbuka ziara zake katika jamii za mbali akiwa na timu za huduma za M-koba za MSI, Mapunda aliwapongeza wahudumu wa afya kwa kujitolea kwao licha ya mazingira magumu ili kuhakikisha wanawake na wasichana wanapata huduma zinazookoa maisha.

Alithibitisha tena dhamira ya Serikali ya Uingereza ya kuendelea kuunga mkono uwekezaji kwa vijana na kusisitiza kuwa uongozi imara wa Serikali, ushirikiano endelevu na kuendelea kuunga mkono huduma za afya ya uzazi ni mambo muhimu katika kuboresha matokeo ya afya na kuhakikisha jamii zinakuwa na mustakabali wenye afya bora.




 

 

Na.Mwandishi Wetu

Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela ( NM- AIST) inatumia mbio za marathon kama moja ya mikakati ya kupata fedha za kutoa ufadhili wa masomo kwa wanawake na wasichana ili kuongeza ushiriki wao katika masomo ya Sayansi, Teknolojia, Hisabati na Ubunifu (STEM).

Hayo yamebainishwa Julai 19, 2026 Jijini Arusha wakati wa Maadhimisho ya Mbio za Taasisi hiyo na Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila ambapo amesema kuwawezesha wanawake na wasichana katika masuala ya Sayansi si hisani bali ni uwekezaji wa kimkakati wa Maendeleo ya Taifa

Dkt. Nguvila ameeleza kuwa Dira ya Taifa 2050 inalenga kujenga uchumi wa maarifa unaotegemea ujuzi, utafiti na teknolojia hivyo ametoa wito kwa Taasisi za Elimu ya Juu hususan NM- AIST kuhakikisha tafiti zinazofanyika katika Taasisi hiyoziwe ni zile zizotatua changamoto za wananachi katika sekta za Kilimo, mifugo, madini na viwanda.

​Akizungumza awali katika tukio hilo Makamu Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Prof. Maulilio Kipanyula amesema kuwa mbio hizo zilianzishwa mwaka 2024 kuhamasisha wasichana kusoma masomo ya sayansi na kutimiza ndoto zao za kuwa madaktari, wahandisi na watafiti.

"​Kwa sasa, Mbio za Mandela zimekuwa alama ya mkoa wa Arusha kwa kuchangia ukuaji wa sekta za michezo, elimu, sayansi, afya na utalii. Tukio hili limeweka msingi imara wa kujenga taifa lenye ujumuishi, mshikamano, na kuandaa kizazi kipya cha wanasayansi na wabunifu wasichana na wanawake," amesema Prof Kipanyula

Mbio hizo zilizohusisha umbali wa kilomita 2.5, 5 10 na 21 zimevuta ushiriki mkubwa wa jamii kutoka ndani na nje ya nchi, na kufanya azma ya kuifanya Arusha kitovu cha sayansi na ubunifu barani Afrika kuwezekana.

Mbio za NM- AIST za Mwaka 2026 zina kauli mbiu isemayo Jitihada kwa Sayansi Hatua kwa Mafanikio.


Top News