Na Farida Mangube Morogoro

Bodi ya Maji ya Bonde la Wami-Ruvu imewatoa hofu wakazi wa Manispaa ya Morogoro kuwa maji ya Bwawa la Mindu ni salama, kwani kemikali iliyomwagika haikufikia chanzo cha maji.

Wasiwasi huo ulizuka kufuatia ajali ya lori lililokuwa likisafirisha kemikali aina ya sulphur kuacha njia na kugonga miti mita 300 kutoka bwawa la Mindu mtaa wa mikoroshini Kata ya Mindu barabara kuu ya Morogoro–Iringa.

Mkurugenzi wa Bonde la Maji bonde la Wami-Ruvu, Mhandisi Elibariki Mmasi, amesema hatua za haraka zilizochukuliwa na wataalamu zilisaidia kuzuia kemikali hiyo kusambaa hadi kwenye chanzo cha maji.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Morogoro (MORUWASA), CPA Sais Kyejo, amesema uchunguzi wa awali umebaini kuwa hakuna madhara yaliyobainika katika ubora wa maji yanayosambazwa.

“Wananchi waendelee kutumia maji bila hofu,” amesema Kyejo.

Naye Meneja wa Kanda ya Kati wa Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Bi Magdalena Mtenga, amesema hadi sasa hakuna madhara yaliyoripotiwa kwa wananchi, licha ya kemikali hiyo kuwa hatarishi endapo itashughulikiwa bila tahadhari.

Ameeleza kuwa sulphur ina sifa ya kuwaka na hata kulipuka, pamoja na kusababisha muwasho wa ngozi au koo, lakini hali hiyo haikutokea wakati wa operesheni ya kuiondoa katika eneo la ajali.

Taasisi mbalimbali zikiwemo Bonde la Wami-Ruvu, MORUWASA, Baraza la Taifa la Usimamizi wa Mazingira (NEMC) pamoja na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji zilishiriki kuondoa kemikali hiyo kwa usalama.

Meneja wa NEMC Kanda ya Morogoro na Rufiji, Arnold Mapinduzi, amesema kemikali hiyo itateketezwa kwa mujibu wa sheria ili kulinda mazingira.

Ajali hiyo ni ya tatu ndani ya mwezi mmoja kuhusisha usafirishaji wa kemikali aina ya sulphur Barabara kuu ya Morogoro - Iringa hali inayochochea haja ya kuimarisha usalama wa usafirishaji wa kemikali hatarishi.





MHESHIMIWA Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameihakikishia Jamhuri ya Belarus kuwa Tanzania itaendeleza ushirikiano na nchini hiyo na kwamba amewaalika wawekezaji na wafanyabiashara kuja nchini  kuangalia fursa za uwekezaji katika sekta za kilimo, uvuvi, elimu na afya.

 Kauli hiyo imetolewa leo (Jumanne, Aprili 28, 2026) na Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba alipokutana na Waziri wa Mambo ya Nje wa Belarus, Maxim Ryzhenkov, Ofisi Ndogo ya Waziri Mkuu, Magogoni jijini Dar es Salaam.

Pia, Dkt. Mwigulu amepokea kwa niaba ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan mwaliko wa ziara ya kikazi nchini Belarus wa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Belarus, Mheshimiwa Alexander Lukashenko.

 Waziri Mkuu, amesema Serikali imeboresha mazingira ya uwekezaji na biashara, pia Tanzania kibiashara ipo katika eneo la kimkakati kijiografia kwa kuwa ni kitovu cha Mataifa ya Ukanda wa Afrika Mashariki na ya Kusini mwa Afrika.

“Ni kutokana na umuhimu huo, Tanzania kupitia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050 imejiwekea lengo la kuwa tegemeo la kanda hizo katika sekta ya kilimo sanjari na sekta ya afya ambayo Dira 2050 inataka Tanzania ijitosheleze katika uzalishaji wa dawa kufikia asilimia 80 ifikapo mwaka 2050.” Amesema Waziri Mkuu.

Waziri Mkuu amesisitiza kuwa ushirikiano kati ya Tanzania na Belarus katika sekta hizo utakuwa na matokeo chanya na ya haraka kutokana na nchi ya Belarus kupiga hatua katika sekta hizo, hasa matumizi ya teknolojia kwenye viwanda mbalimbali vikiwemo vya dawa na zana za kilimo. 

“Tutaangalia uwezekano wa kubadilishana wataalam kama sehemu ya mafunzo kwa vitendo, ambapo Tanzania itatuma wataalam wa kilimo nchini Belarus ili wapate ujuzi, mfano katika teknolojia ya uundaji matrekta ya kisasa na zana nyingine za kilimo.” Ameongeza Waziri Mkuu.

Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Nje wa Belarus, Maxim Ryzhenkov ameeleza kuwa Serikali ya Belarus ipo tayari kushirikiana na Tanzania katika sekta mbalimbali zikiwemo kilimo, mifugo, uvuvi, elimu, sayansi na teknolojia.

“Nimefanya mazungumzo na mawaziri wa sekta muhimu hapa Tanzania, wakiwemo Waziri wa Elimu, Waziri wa Ulinzi na Waziri wa Mifugo na Uvuvi, ambapo kwenye eneo la uvuvi tumeona fursa ya kuwa wananuzi wazuri wa mazao ya baharini kwani Tanzania yanapatikana kwa wingi.” 

Ameongeza kuwa Belarus na Tanzania zinatarajiwa kusaini mikataba ya makubaliano (MoU) kuhusu kuwa na Tume ya Pamoja ya Biashara kati ya Tanzania na Belarus.“Makubaliano hayo yatawawezesha wafanyabiashara wa Tanzania na wa Belarus kuendesha shughuli zao kirahisi na hivyo kuchochea ukuaji wa uchumi.”

Wakati akikabidhi ujumbe wa mwaliko wa ziara ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan nchini Belarus, Waziri wa Mambo ya Nje wa Belarus, Maxim Ryzhenkov amesema pia Waziri Mkuu wa Belarus, Alexander Turchin anatarajiwa kufanya ziara ya kikazi nchini Tanzania hivi karibuni.










📌 Yapongeza REA na SUMA JKT kwa utekelezaji thabiti

📌 Bilioni 3.2 kukamilisha miradi Ludewa

Ludewa, Njombe📍

Bodi ya Nishati Vijijini (REB) imeeleza kuridhishwa na kasi na ubora wa utekelezaji wa miradi ya usambazaji umeme katika maeneo ya mwambao wa Ziwa Nyasa yaliyopo katika Wilaya za Ludewa na Makete, ikipongeza juhudi za Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa kushirikiana na mkandarasi, Shirika la Uzalishaji Mali la Jeshi la Kujenga Taifa (SUMA JKT).

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya ziara ya ukaguzi katika maeneo ya Nkanda na Lumbila, Mjumbe wa Bodi, Florian Haule, alisema Bodi imejionea maendeleo makubwa ya mradi huo unaolenga kusambaza umeme kwa wananchi waishio katika maeneo yenye changamoto za kijiografia wilayani Ludewa na Makete.

Alieleza kuwa pamoja na ugumu wa miundombinu katika ukanda huo wa Bonde la Ufa, utekelezaji wa mradi unaendelea kwa kasi ya kuridhisha, ambapo kazi ya usimikaji wa nguzo imefikia hatua kubwa na kinachoendelea sasa ni uvutaji wa nyaya.

“Tumefurahishwa na hatua iliyofikiwa. Vifaa vyote muhimu vimeshafikishwa na katika siku chache zijazo tutaanza kushuhudia ufungaji wa transfoma,” alisema Haule.

Kwa mujibu wa Haule, mkandarasi SUMA JKT ameihakikishia Bodi kukamilisha kazi hiyo ifikapo Julai, 2026; ahadi inayotoa matumaini kwa wananchi wenye uhitaji mkubwa wa huduma ya umeme katika maeneo hayo.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Mipango na Utafiti REA, Mhandisi Yusuph Ismail, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Hassan Saidy, alisema hatua inayofuata ni usimikaji wa transfoma na ujenzi wa njia za umeme za msongo mdogo (LV) ili kuanza kuunganisha wateja wa awali.

Alibainisha kuwa katika kitongoji cha Nkanda, kazi ya usimikaji wa nguzo kwa umbali wa takribani kilometa tisa imekamilika kwa kiwango kikubwa, huku matarajio yakiwa ni kuwasha umeme ifikapo Mei 25, mwaka huu.

“Tunawahimiza wananchi kufanya maandalizi ya ndani ya nyumba (wiring) ili waweze kuunganishiwa umeme mara moja pindi huduma itakapoanza,” alisisitiza Mhandisi Ismail.

Aliongeza kuwa upatikanaji wa umeme utakuwa kichocheo muhimu cha maendeleo ya kiuchumi katika ukanda wa Ziwa Nyasa, hususan kwa shughuli za uvuvi, kwa kuwezesha matumizi ya teknolojia za kisasa za kuhifadhi samaki na kuongeza thamani ya mazao hayo.

Aidha, huduma za kijamii ikiwemo shule, vituo vya afya, nyumba za ibada na ofisi za vijiji zinatarajiwa kunufaika moja kwa moja na mradi huo, hali itakayoboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Naye Mkurugenzi Mwendeshaji wa kampuni ya umeme ya SUMA JKT, Meja James Mhame, ambaye pia ni Meneja wa Mradi huo, alisema utekelezaji unaendelea vizuri huku zaidi ya asilimia 80 ya kazi ya awamu ya kwanza ikiwa imekamilika.

“Hatua inayofuata ni uvutaji wa nyaya kwa kiwango kikubwa pamoja na ufungaji wa transfoma ili kuanza kusambaza umeme kwa wananchi wa Nkanda na Lumbila,” alisema Meja Mhame.

Kwa upande wake, Meneja Msimamizi wa Miradi kutoka REA, Mhandisi Deogratius Nagu, alisema Serikali imetenga shilingi bilioni 3.2 kwa ajili ya kutekeleza mradi huo katika Wilaya ya Ludewa, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuhakikisha vitongoji vyote vinafikiwa na huduma ya umeme.

Alifafanua kuwa changamoto za kijiografia katika ukanda huo, ikiwemo usafirishaji wa vifaa kwa njia ya maji na kupandishwa milimani, ndizo zilizosababisha REA kulichagua jeshi kutekeleza mradi huo.

“Maelekezo ya Bodi yametutaka kuhakikisha wananchi wote walio tayari wanaunganishwa na umeme kabla mkandarasi hajaondoka. Tumejipanga kuyatekeleza kikamilifu,” alisema Mhandisi Nagu.

Miradi hiyo ni sehemu ya jitihada za Serikali kupitia REA za kuhakikisha upatikanaji wa umeme unawafikia wananchi wote wa vijijini, hususan wale wanaoishi katika maeneo ya pembezoni kama ukanda wa Ziwa Nyasa.











Na Mwandishi wetu- DODOMA

Katibu Tawala Mkoa wa Dodoma, Dkt. Khatibu Kazungu, amesema Ofisi yake ikishirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu Idara ya Menejimenti ya Maafa ipo katika hatua ya kuanzisha Kituo cha Operasheni ya Dharura katika Mkoa ikiwa ni utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Usimamizi wa Maafa ya mwaka 2004.

Dkt. Kazungu ameyasema hayo leo tarehe 27 Aprili,2026 jijini Dodoma kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma wakati akifungua mafunzo ya siku nne ya kujiandaa na kukabiliana na maafa kwa Timu ya kukabiliana na dharura ya Mkoa ambayo yameandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa pamoja na uanzishaji wa kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura cha Mkoa.


Aidha, Dkt. Kazungu ameshukuru ujio wa elimu hiyo ndani ya Mkoa wa Dodoma akisema itasaidia kuwajenga kielimu Maafisa wa Mkoa ili waweze kupeleka elimu katika ngazi za Wilaya.


"Elimu hii itasaidia kuongeza ujuzi na weledi kwa Maafisa wa Mkoa kwani majanga haya yamekuwa na madhara mengi kwa jamii," alisema Dkt. Kazungu.


Pia, alisisitiza ukusanyaji wa taarifa kwa wakati na kabla ya majanga ili kurahihisisha kuyakabili pamoja na kuboresha mawasiliano ya karibu baina ya wananchi na Maafisa wa Mkoa.


"Lazima kuwepo ushirikiano baina yetu na Wananchi ili tuweze kupambana na maafa ndani ya Mkoa wetu wa Dodoma," alisisitiza.

Awali Kaimu Mkurugezi Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Kanali Selestine Masalamadu aliupongeza Mkoa wa Dodoma kwa kuwa tayari kupokea elimu ya maafa na majanga na kusema kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Idara hiyo ina jukumu la kuratibu shughuli za Kuzuia, Kupunguza Athari, Kujiandaa, Kukabiliana na Kurejesha hali baada ya maafa.

Vilvile, alisema kuwa Ofisi inaendelea kuratibu uanzishaji na uendeshaji wa Vituo vya Operesheni na Mawasiliano ya Dharura vya Mikoa pamoja na Timu za kukabiliana na dharura , ikiwa ni utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Usimamaizi wa Maafa ya Mwaka 2004, Sheria ya Usimamaizi wa maafa Na. 6 ya mwaka 2022 na kanuni zake.


“Lengo la mafunzo haya ni kuimarisha uwezo wa Mkoa kuratibu shughuli za usimamaizi wa maafa ili kupunguza madhara wakati wa dharura. Mafunzo haya yatawajengea uwezo washiriki katika maandalizi, uratibu wa taarifa, mwitikio wa haraka, usimamizi rasilimali na utoaji wa huduma kwa waathirika,” alifafanua Kanali Masalamadu.


Aidha, alibainisha kwamba kila Mkoa unatakiwa kuwa na chumba maalum kwa ajili ya kuratibu shughuli za maafa na dharura huku akihimiza kuharakishwa kwa upatikanaji wa chumba chenye sifa stahiki kuwezesha uanzishwaji kamili wa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura Mkoa wa Dodoma.

Na Mwandishi wetu Dodoma

Serikali ya Tanzania imepiga hatua nyingine muhimu katika kuimarisha miundombinu ya usafiri baada ya kusaini mikataba ya ufadhili na ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) kwa vipande vya Makutupora–Tabora (Lot 3) na Tabora–Isaka (Lot 4), kwa ushirikiano na mataifa ya Italy, Sweden na Poland.

Akizungumza katika hafla ya utiaji saini iliyofanyika leo Aprili 28, 2026, Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa, amesema mradi huo ni hatua ya kimkakati katika kukuza uchumi wa taifa na kuboresha huduma za usafiri nchini. Alieleza kuwa reli hiyo ya kisasa itaongeza ufanisi katika usafirishaji wa mizigo na abiria, sambamba na kupunguza gharama za usafiri.

Aidha, Profesa Mbarawa amesisitiza kuwa kukamilika kwa vipande hivyo kutachochea ukuaji wa biashara kwa kuunganisha mikoa ya kati na Kanda ya Ziwa. Hatua hiyo pia itarahisisha mawasiliano ya kiuchumi na nchi jirani, na hivyo kuifanya Tanzania kuwa lango muhimu la biashara katika ukanda huo.

Mradi wa SGR unaendelea kuwa kichocheo kikubwa cha maendeleo ya kiuchumi nchini, ukiwa na matarajio ya kupunguza muda wa safari, matumizi ya mafuta, pamoja na kupunguza uchafuzi wa mazingira. Reli hiyo ya kisasa pia inalenga kuongeza ushindani wa Tanzania kama kitovu cha usafirishaji katika Afrika Mashariki na Kati.

Zaidi ya hayo, utekelezaji wa mradi huu unatarajiwa kufungua ajira kwa maelfu ya Watanzania, kuongeza mapato ya ndani, na kuimarisha sekta nyingine kama utalii, biashara na viwanda. Hii inaonesha dhamira ya serikali ya kuendelea kuwekeza katika miradi mikubwa ya kimkakati yenye tija kwa maendeleo ya wananchi na taifa kwa ujumla.









 

 

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Daniel Mushi, amesema upatikanaji wa mabasi ya watumishi yatasaidia sana katika kuweka mazingira salama na wezeshi ya utendaji.

Amesema hatua hiyo inaonesha dhamira ya dhati ya Serikali katika kujali watumishi na kuboresha mazingira ya kazi.

Amesisitiza kuwa watumishi ni nguzo kuu ya kufikia malengo kwani ndio watekekezaji wa mipango na maono wizara hivyo, Wizara inaendelea kuweka mazingira stahiki na jumuishi kwa watumishi wote.

"Rais wetu amesisitiza kazi iende sambamba na kujali utu, na hivi ndio tunatekeleza kauli mbiu ya Kazi na Utu tunasonga mbele kwa kuweka mazingira yanayovutia utendaji kwa watumishi" amesema Prof. Mushi.

Prof. Mushi amewahimiza watumishi kutumia mabasi hayo na kuyatunza ili yaweze kurahisisha utendaji kazi na kutumika kwa muda mrefu.

Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimaliwatu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Edith Rwiza amesema ununuzi wa mabasi matatu (3) mapya kwa ajili ya usafiri wa watumishi ni hatua muhimu ya kuboresha mazingira ya kazi kwa Wizara.

Akizungumza jijini Dodoma Aprili 28, 2026 katika uzinduzi wa mabasi ya watumishi, Mkurugenzi huyo amesema mabasi hayo yamenunuliwa na Wizara kwa kushirikiana na Mradi wa Kuimarisha na Kuboresha Elimu ya Awali na Msingi Tanzania Bara (BOOST) kwa zaidi ya Shilingi milioni 500 kwa lengo la kuwezesha watumishi katika safari za kila siku za kwenda kazini na kurudi nyumbani pamoja na ziara za kikazi.

"Kabla ya hatua hii, watumishi walilazimika kutumia kati ya shilingi 10,000 hadi 15,000 kwa siku kufika ofisini hali iliyoleta ugumu wa maisha na kupunguza morali ya kazi" amesema Dkt. Rwiza

Mkurugenzi Rwiza amesema upatikanaji wa mabasi haya ni sehemu ya jitihada za wizara kuhakikisha watumishi wanafanya kazi katika mazingira bora na yenye ufanisi.

Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikalin na Afya (TUGHE), Bw. Moshi Kisinga ameushukuru uongozi wa Wizara hiyo kwa kununua magari kwa ajili ya watumishi.

"Kwa niaba ya watumishi wenzangu tumepokea magari haya kwa furaha na hakika tumeondokana na changamoto kubwa ya usafiri", amesema Kisinga.

Ametoa rai kwa watumishi kufanya kazi kwa juhudi na maarifa akisisitiza uwajibikaji katika majukumu ya kila siku.


Top News