Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma
Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeendelea kuandika historia katika sekta ya miundombinu baada ya kufanikisha ujenzi wa zaidi ya kilometa 1,495 za barabara kwa kiwango cha lami pamoja na madaraja makubwa 18 ndani ya kipindi cha miaka mitano.
Mafanikio hayo yametajwa kuwa sehemu ya mageuzi makubwa yanayoendelea kufanyika nchini katika kuimarisha sekta ya uchukuzi na usafirishaji, hatua inayolenga kurahisisha huduma za kijamii, kukuza biashara na kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi wa Taifa.
Akizungumza bungeni jijini Dodoma leo Jumatano Mei 20, 2026 wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Ujenzi kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, amesema Serikali imepiga hatua kubwa katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya barabara na madaraja katika maeneo mbalimbali nchini.
Amesema katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya Sita, jumla ya kilometa 1,495.45 za barabara zimejengwa kwa kiwango cha lami huku madaraja makubwa 18 yakijengwa au kuendelea kujengwa, jambo ambalo limeongeza ufanisi wa usafiri na kuchochea shughuli za kiuchumi mijini na vijijini.
Kwa mujibu wa Waziri Ulega, mtandao wa barabara za kitaifa unaosimamiwa na TANROADS umefikia kilometa 37,734.41, ambapo kati ya hizo kilometa 12,225.26 tayari zimejengwa kwa kiwango cha lami.
Ameeleza kuwa mafanikio hayo yanaonesha namna Serikali ilivyoongeza kasi ya uwekezaji katika sekta ya miundombinu ikilinganishwa na miaka ya nyuma, akibainisha kuwa wakati Tanzania inapata uhuru mwaka 1961, nchi ilikuwa na kilometa 1,360 pekee za barabara za lami.
Aidha, amesema kuanzia Serikali za Awamu ya Kwanza hadi Awamu ya Tano, jumla ya kilometa 9,369.81 za barabara za lami zilikuwa zimejengwa, huku Serikali ya Awamu ya Sita ikiendelea kuongeza kasi kubwa ya utekelezaji wa miradi hiyo kwa muda mfupi.
“Serikali imeendelea kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika sekta ya miundombinu kwa lengo la kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za usafiri na usafirishaji pamoja na kufungua fursa za kiuchumi katika maeneo mbalimbali ya nchi,” amesema Waziri Ulega.
Katika utekelezaji wa bajeti ya mwaka wa fedha 2025/2026, Waziri huyo amesema Wizara ya Ujenzi ilipanga kujenga na kukarabati barabara kuu na za mikoa zenye urefu wa kilometa 450 kwa kiwango cha lami pamoja na kilometa 820 kwa kiwango cha changarawe.
Hata hivyo, hadi kufikia Aprili 2026, Serikali ilikuwa imefanikiwa kukamilisha ujenzi na ukarabati wa kilometa 243.13 za barabara kwa kiwango cha lami pamoja na kilometa 94.36 kwa kiwango cha changarawe.
Kwa upande wa madaraja, Waziri Ulega amesema Serikali imekamilisha ujenzi wa madaraja tisa ambayo ni Mitomoni mkoani Ruvuma, Mirumba mkoani Katavi, Nzali mkoani Dodoma, Doma, Chakwale na Nguyami mkoani Morogoro, Mkili mkoani Ruvuma, Kalebe mkoani Kagera pamoja na Itembe mkoani Simiyu.
Amesema ujenzi wa madaraja mengine 11 unaendelea katika maeneo mbalimbali nchini, huku Serikali ikiendelea na maandalizi ya utekelezaji wa miradi mipya ya madaraja 13.
Mbali na hilo, Serikali pia inaendelea na kazi za upembuzi yakinifu pamoja na usanifu wa kina kwa baadhi ya miradi ya madaraja yenye lengo la kuboresha miundombinu ya usafiri katika maeneo yenye changamoto za mawasiliano wakati wa mvua na mafuriko.
Waziri Ulega amesema maboresho hayo ya miundombinu yanaendelea kuwa chachu ya ukuaji wa sekta mbalimbali ikiwemo biashara, kilimo, utalii na uwekezaji, huku wananchi wakinufaika na kupungua kwa muda wa safari pamoja na gharama za usafirishaji wa bidhaa na huduma.
Amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kusimamia utekelezaji wa miradi ya kimkakati kwa kuhakikisha barabara na madaraja yanajengwa kwa viwango vinavyokidhi mahitaji ya sasa na ya baadaye ya Watanzania.
“Dhamira ya Serikali ni kuhakikisha mtandao wa barabara unaendelea kuimarika ili kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini,” amesema Waziri Ulega.


















.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)

.jpeg)















.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)