Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema mkataba wa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa mradi wa Barabara ya Kitusha–Kinampanda–Kisana–Kisiriri umeshasainiwa, hatua inayofungua njia ya kuanza kwa utekelezaji wa mradi huo unaotarajiwa kubadilisha shughuli za usafiri na uchumi katika maeneo ya Wilaya ya Iramba.

Dkt. Mwigulu amesema hayo leo, Jumapili Juni 14, 2026, wakati akizungumza, kusikiliza na kutatua changamoto za wananchi wa Tarafa ya Kinampanda katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Uwanja wa Chuo cha Ualimu Kinampanda, Wilaya ya Iramba mkoani Singida.

Amesema Serikali imekamilisha hatua muhimu ya upatikanaji wa fedha za mradi huo na kwamba changamoto iliyobaki sasa ni kukamilisha taratibu za kumpata mkandarasi atakayetekeleza ujenzi huo.

“Leo tunavyoongea, mkataba wa upatikanaji wa fedha umeshasainiwa. Kwa hiyo fedha si tatizo tena. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa na Mwenyekiti wa Halmashauri ambao walishuhudia kusainiwa kwa mkataba huo,” amesema Dkt. Mwigulu.

Amesema barabara hiyo itaanzia Kitusha, kupita Kinampanda, Galangala, Kisana na kuunganishwa na Kisiriri kabla ya kuelekea Sibiti, hatua itakayorahisisha mawasiliano na usafirishaji wa watu na bidhaa katika ukanda huo.

Waziri Mkuu amesema mradi huo utatekelezwa kwa kiwango cha kisasa na unatarajiwa kuwa miongoni mwa barabara bora zaidi mkoani Singida.

“Barabara hii huenda ikawa moja ya barabara bora kuliko zote hapa mkoani Singida. Itakuwa ni barabara ya kisasa kweli kweli,” amesema.

Akitoa ufafanuzi wa hatua za utekelezaji wa mradi huo, Meneja wa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) Mkoa wa Singida, Mhandisi Claver Mwinuka amesema tayari mchakato wa kumpata mshauri elekezi unaendelea na unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Juni mwaka huu.

Amesema baada ya kukamilika kwa michoro na nyaraka za zabuni, Serikali itaanza mchakato wa kumpata mkandarasi huku matarajio yakiwa ni mkandarasi huyo kupatikana ifikapo mwezi Septemba mwaka huu.

Mhandisi Mwinuka amesema barabara hiyo ina urefu wa kilometa 38.5 na itajengwa kwa upana wa mita 9.5, tofauti na barabara nyingi za TARURA ambazo hujengwa kwa upana wa mita 8.5.

Aidha, amesema barabara hiyo itakuwa na taa zaidi ya 400 pamoja na vituo vya mabasi vya kisasa vitakavyoboresha huduma za usafiri kwa wananchi.

Wakati huohuo, Dkt. Mwigulu amesema Serikali itaendelea kuimarisha huduma za afya katika Tarafa ya Kinampanda kwa kupeleka gari jipya la wagonjwa (ambulance) katika Kituo cha Afya Kinampanda ndani ya wiki moja hadi mbili.

Amesema hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuboresha huduma za afya kwa wananchi kufuatia kukamilika kwa ujenzi wa Kituo cha Afya Kinampanda kupitia mpango wa Serikali wa kujenga vituo vya afya katika kila tarafa.

“Leo kama sehemu ya shukrani, nawaletea ambulance mpya. Itakuwepo hapa kituoni ili iweze kuwasaidia wananchi wa Kinampanda,” amesema.

Aidha, Dkt. Mwigulu ambaye pia ni Mbunge wa Iramba Magharibi amesema Serikali inaendelea na maandalizi ya utekelezaji wa miradi mingine ya barabara katika Wilaya ya Iramba ikiwemo Shelui–Nkongilangi–Tulya–Kidaru, Mtoa–Mtekente–Urugu–Mlandala–Sepuka pamoja na Iguguno–Nduguti–Gumanga–Sibiti ambayo ipo katika hatua mbalimbali za usanifu na maandalizi ya utekelezaji.



Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amemuagiza Waziri wa Maji kwenda Mkoa wa Mwanza kushughulikia mara moja changamoto ya upatikanaji wa maji inayowakabili wananchi wa mkoa huo na kuhakikisha huduma hiyo inarejea kwa haraka.

Dkt. Mwigulu ametoa maelekezo hayo leo, Jumapili Juni 14, 2026, wakati akizungumza, kusikiliza na kutatua changamoto za wananchi wa Tarafa ya Kiomboi katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Uwanja wa Shule ya Msingi Lulumba, Wilaya ya Iramba mkoani Singida.

Amesema amepokea taarifa kuhusu changamoto ya maji katika Mkoa wa Mwanza na tayari amemuelekeza Waziri mwenye dhamana ya maji kwenda eneo husika kusimamia upatikanaji wa suluhisho la haraka.

“Nimemtuma Waziri aende haraka Mwanza akasimamie jambo lile mpaka maji yapatikane. Sisi watu wa Singida tunataka tupate maji toka Mwanza. Simiyu tunataka tupate maji toka Mwanza. Dodoma tunataka tupate maji toka Mwanza. Tabora, wengine wameshaanza kupata maji toka Mwanza. Leo kuja kuambiwa Mwanza, pale pale lilipo Ziwa Victoria, pana shida ya maji. Hili ni jambo ambalo haliwezi kueleweka, na wala hatuwezi kulielewa,” amesema Dkt. Mwigulu.

Amesema hakuna sababu ya wananchi kuendelea kukosa huduma hiyo wakati chanzo cha maji kinajulikana na miundombinu ya mradi ipo.

“Hatutaki ngonjera za maneno. Hawa wanasema si bomba limekuwaje, hawa wanasema si umeme umekuwaje. Chanzo sisi tunajua kiko pale, hatuna shida ya chanzo cha maji, na mradi upo, na maji yapo. Haya mambo mengine ni ya ngonjera, mimi sitaki kuyasikia,” amesema.

Waziri Mkuu amewataka wataalamu wa sekta ya maji pamoja na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kufanya kazi kwa pamoja na kuhakikisha wananchi wanapata huduma hiyo kwa haraka.

“Mkuu wa Mkoa awatafute wataalamu wake, awatafute TANESCO na wataalamu wa maji. Wachimbe kiini cha tatizo na wakeshe mpaka wananchi wapate maji. Kunapopambazuka kesho nipate majawabu kwamba maji yamepatikana,” amesema.

Juni 9, 2026, Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mwanza (MWAUWASA) ilitoa taarifa kwa umma kuhusu upungufu wa huduma ya maji uliosababishwa na hitilafu za umeme zilizokuwa zikijitokeza mara kwa mara.

Wakati huohuo, Dkt. Mwigulu amesema Serikali imejipanga kuhakikisha changamoto ya upatikanaji wa maji katika Tarafa ya Kiomboi na maeneo mengine ya Wilaya ya Iramba inapata ufumbuzi wa kudumu kupitia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maji pamoja na uwekezaji mkubwa unaoendelea kufanywa katika sekta hiyo nchini.

Amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeweka kipaumbele maalum katika sekta ya maji kwa kutekeleza miradi ya kimkakati inayolenga kuongeza upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi.

“Niwahakikishie kwamba hili ni eneo ambalo Mheshimiwa Rais ameliwekea kipaumbele cha hali ya juu kwa sababu maji ni uhai, maji ni maisha. Tulihangaika kupata chanzo cha uhakika cha maji na sasa kimepatikana, hatua mbalimbali zinaendelea ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma hiyo kwa uhakika,” amesema.

Aidha, amesema Serikali inaendelea na utekelezaji wa mpango wa Gridi ya Taifa ya Maji pamoja na kuimarisha uwezo wa uchimbaji wa visima, ujenzi wa mabwawa na upimaji wa vyanzo vya maji ili kukabiliana na changamoto ya maji katika maeneo mbalimbali nchini.

Dkt. Mwigulu ambaye pia ni Mbunge wa Iramba Magharibi amesema Serikali inaendelea na usanifu wa barabara ya Kiomboi–Kisiriri–Sibiti kwa lengo la kuijenga kwa kiwango cha lami na kuboresha mawasiliano kati ya wananchi wa maeneo hayo na maeneo jirani.

Aidha, amesema usanifu wa barabara ya Kitusha–Galangala–Kisana–Kinampanda–Kisiriri umekamilika, huku Serikali ikiendelea na maandalizi ya utekelezaji wa miradi mingine ya barabara katika Wilaya ya Iramba ili kurahisisha shughuli za kijamii na kiuchumi.

Pia amesema usanifu wa daraja la kuunganisha eneo la Hospitali ya Kiomboi na maeneo ya Meli pamoja na Iguguno umekamilika na hatua zinazofuata ni kumpata mkandarasi kwa ajili ya kuanza utekelezaji wa mradi huo.

Sambamba na hilo, Dkt. Mwigulu amesema Serikali inaendelea na maandalizi ya kuanzisha Chuo Kikuu katika eneo la Kiomboi baada ya eneo lililotengwa kuridhiwa na wataalamu husika.

“Hapa Kiomboi tutakuwa na Chuo Kikuu. Eneo limekaguliwa na kuridhiwa na hatua za utekelezaji zinaanza,” amesema.

Amesema pindi ujenzi wake utakapokamilika, Chuo Kikuu hicho kinatarajiwa kuanza kwa awamu ya kwanza kwa uwezo wa kuhudumia wanafunzi takribani 10,000.




Na Mwandishi wetu

Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Utawala na Rasilimali Watu Ofisi ya Waziri Mkuu,Sera, Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu Vedastina Kagombora amesema kuwa Suala la ujumuishaji sio jukumu la Sekta moja bali ni la kila Wizara kushirikiana ili kuweka mazingira rafiki katika upatikanaji wa huduma muhimu ikiwemo afya,Elimu na Miundombinu rafiki kwa watu wenye ulemavu.

Vedastina ameyasema hayo Jijini Dodoma katika kikao kilichoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu,Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu na Wawakilishi wa Madawati ya wenye ulemavu wa Wizara zote na baadhi ya Taasisi za Serikali.

Ambapo amesema kuwa umuhimu wa madawati haya ya kuleta haki,ushiriki wa watu wenye ulemavu yanayojumuisha katika mipango na Sera,Bajeti,Programu na shughuli zote za maendeleo ni za Wizara husika na sio kuyaacha yashughulikiwe na Ofisi inayoratibu masuala ya watu wenye ulemavu pekee.

"Ni muhimu kutambua kuwa ujumuishaji sio jukumu la Sekta au Wizara moja pekee bali ni wajibu na jukumu la kila Wizara na sisi wote kuendelea kushirikiana katika kuweka mazingira rafiki yanayowezesha upatikanaji wa huduma zote muhimu ikiwemo Elimu jumuishi,Huduma za Afya,Ajira,Teknolojia Saidizi,Huduma za Kijamii,Miundombinu Fikivu pamoja na ushiriki wa watu wenye ulemavu katika kutoa maamuzi yanayoweza kuwafikia watu weny Ulemavu".

Aidha Vedastina amebainisha mafanikio makubwa waliyoyapata katika kuratibu masuala ya watu wenye ulemavu kuwa pamoja na mapitio ya Sera ya watu wenye ulemavu,kuunda madawati ya watu wenye ulemavu katika Wizara mbalimbali,kupata mikopo ya Serikali na pia kutengeneza mfumo wa taarifa za watu wenye ulemavu ambapo wanasajiliwa na kupata namba ya usajili ili kuwatambua kwa urahisi mahali walipo.

Kwa upande wake Mdoka Omary ambaye ni Mtakwimu Mwandamizi kutoka Ofisi wa Taifa ya Takwimu ameeleza kuwa Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022 iliendelea kutumia maswali sita kulingana na Mwongozo wa Kimataifa wa Washington Group pamoja na nyongeza ya maswali mengine ya ulemavu kutoka SHIVYAWATA ambapo Maswali yaliyoulizwa kwenye sehemu ya hali ya ulemavu, ni Ualbino, Kuona, Kusikia, Kutembea/kupanda ngazi, Kukumbuka/kufanya vitu kwa umakini, Kujihudumia, Kuwasiliana na “Aina Nyingine ya Ulemavu” ambapo Aina nyingine ya ulemavu ilijumuisha maswali ya ulemavu wa Mdomo Sungura, Kichwa Kikubwa, Mgongo Wazi; Kuumia Uti wa Mgongo; Kifafa; Mabakamabaka ya Ngozi, Mbalanga (Storiasis); Usonji (Autism); Matatizo ya Afya ya Akili; Ulemavu wa Akili; Mtu Mwenye Kimo Kifupi; Ukoma na mtu Mwenye Kibiongo.

Aidha, kwa mara ya kwanza waliuliza maswali yanayohusu chanzo cha ulemavu na iwapo mtu mwenye ulemavu anatumia kifaa saidizi, na Kwa mujibu wa Matokeo ya Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka huo wa 2022, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilikuwa na watu wenye ulemavu 5,347,397,na kiwango cha ulemavu nchini kiliongezeka kutoka asilimia 9.3 mwaka 2012 hadi asilimia 11.2 mwaka 2022.

Naye Harun Harun ambaye ni Afisa Ustawi wa Jamii kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI,amesema kuwa Ofisi hiyo kupitia sektretarieti za Mikoa na Halmashauri kuna Mikakati ambayo inafanyika ya kuwabaini watu wenye ulemavu wa kila aina na pia kutenga bajeti kwa makundi haya ambapo bajeti imekuwa ikiongezeka mwaka hadi mwaka.

Ambapo pia Ofisi hiyo imekuwa na kamati katika ngazi za Halmashauri za watu wenye ulemavu ambazo zimeundwa kwenye Mikoa yote 26 Halmashauri 184 na kata zaidi ya 3,400 ili kubaini na kutambua changamoto wanazokutana nazo watu hawa wenye ulemavu ili Maafisa Ustawi waweze kuwafikia kwa urahisi.

Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu ilikondoisha huduma za watu wenye ulemavu katika ngazi za Wizara kwa kuunda madawati ya watu wenye ulemavu mnamo mwaka 2018

Imewakutanisha Wawakilishi hao ili kuwajengea uelewa na kuwakumbusha juu majukumu yao kwa madawati hayo.


Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Mambo ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa Ndg Rabia Abdalla Hamid amesema kuwa Chama cha Mapinduzi kina thamani sana jasho la kila kwa mtanzania, hivyo serikali ya CCM itakikisha kila kundi la kijamii linaguswa ilikuhakikisha linafanikiwa na shughuli zote za kujitafutia mali sambamba na huduma zote zinatokana na serikali.

“Ndugu zangu Wanalindi, CCM inatambua jasho lenu katika kujitafutia mali kupitia shughuli zenu mbalimbali kama kilimo, biashara na ujasiliamali, Serikali ya CCM itahakikisha inaweka mazigira wezeshi ili mnufaike na shughuli zenu zote” Rabia

Aidha  ameyaomba makundi mbalimbali ya kijamii, kuendelea  kushirikiana na CCM kwa ukaribu zaidi, kwa kukipa ushauri, mawazo na kutoa changamoto ili kupitia hayo  serikali ya CCM itazitafutia ufumbuzi.

Ameongezea kuwa Mwenyekiti wa CCM na Rais wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan amedhamiria kuacha tabasamu la kweli kwa kila mtanzania na kwa makundi yote ya kijamii hivyo ni dhamira yake kuona anaugwa  mkono, ili kuliletea maendeleo endelevu Tanzania letu na ndio maana katika mapendekezo ya bajeti kuu ya serikali 2026/2027 imekusudia kutenga asilimia 15 ya mapato ya halmashauri kutoa asilimia 10 ya awali ili kuongeza wigo katika upatikanaji wa mikopo.

Pamoja na hayo ameelekeza Serikali ya Mkoa wa Lindi na Uongozi wa Chama kutenga muda na kufanya mikutano maalum ya kuyasikiliza  makundi ya kijamii.

Ndg Rabia ameyasema hayo leo Juni 14, 2026 Mkoani Lindi alipo kutana na kuongea  na makundi mbalimbali ya kijamii  wakiwemo Wakulima, Wavuvi, Wafugaji, Vyama vya Ushirika, Baba Lishe na Mama Lishe, Maafisa Usafirishaji, wajane, wenye mahitaji maalum, Viongozi wa Serikali za mitaa, viongozi wastaafu pamoja na vikundi mbalimbali vya Ujasiliamali.












RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, leo tarehe 13 Juni 2026, amejumuika na wanafamilia, ndugu, jamaa, wasanii, na mamia ya waombolezaji katika mazishi ya msanii mkongwe, marehemu Issa Joseph Mohamed, maarufu kwa jina la Mzee Onyango, yaliyofanyika Kawe , Wilaya ya Kinondoni, Jijini Dar es Salaam.

Mazishi hayo yamehudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, akiwemo Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma, pamoja na wasanii wa fani mbalimbali na wananchi waliofika kutoa heshima zao za mwisho kwa marehemu.

Mara baada ya kuwasili, Rais Dkt. Mwinyi alisaini kitabu cha maombolezo na kutoa mkono wa pole kwa wanafamilia.

Marehemu Issa Joseph Mohamed alizaliwa tarehe 14 Aprili 1950 na kufariki dunia tarehe 11 Juni 2026, akiwa anapatiwa matibabu katika Hospitali ya Jeshi ya Lugalo, Jijini Dar es Salaam.

Wakati wa uhai wake, marehemu alipata umaarufu mkubwa kupitia kazi zake za filamu na maigizo na kujizolea heshima kubwa miongoni mwa Watanzania kwa jina la Mzee Onyango.

Marehemu amezikwa katika Makaburi ya Kondo, Ununio, Wilaya ya Kinondoni, Jijini Dar es Salaam.
Bwana ametoa na Bwana ametwaa; jina la Bwana lihimidiwe. Amina.
























Na Mwandishi Wetu, Temeke
JAMII imetakiwa kuongeza juhudi za kulinda haki za watoto na kuhakikisha wanapata mazingira salama ya kukua bila ukatili.

Wito huo umetolewa na Mwenyekiti wa UWT Wilaya ya Temeke, Lawama Mikidadi, ambaye alikuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika yaliyofanyika wilayani humo.

Mikidadi amesema maadhimisho hayo ni nafasi ya kuikumbusha jamii wajibu wake wa kusimamia ustawi wa watoto.

“Licha ya jitihada zinazofanywa, bado kuna matukio ya ukatili dhidi ya watoto katika baadhi ya maeneo. Ni wajibu wa wazazi, walezi na jamii kwa ujumla kuhakikisha vitendo hivyo vinatokomezwa,” amesema.

Maadhimisho ya mwaka huu yamefadhiliwa na taasisi za Boys Initiative Tanzania na Miriam Odemba Foundation, ambazo zimetoa pedi na vifaa mbalimbali kwa watoto 300 walioshiriki.

Kwa upande wake, halmashauri ya Manispaa ya Temeke imadhimisha siku hiyo mapema kabla ya tarehe 16 juni mwaka huu.

Kupitia ushiriki huo, Boys Initiative Tanzania imeendelea kupaza sauti ya mtoto wa kiume, huku Miriam Odemba Foundation ikisimama kutetea na kuwezesha mtoto wa kike, taasisi zote mbili zikifanya kazi ya kuhakikisha watoto wanapata ulinzi, fursa na mazingira bora ya kufikia ndoto zao.

Akizungumza na wanafunzi, Mrakibu Msaidizi wa Polisi kutoka Dawati la Jinsia na Watoto Wilaya ya Temeke, Brandina Ndunguru, amewataka watoto kuwa makini dhidi ya watu wanaoweza kutumia zawadi au ahadi mbalimbali kuwashawishi.

“Mtoto anapaswa kulindwa, kusikilizwa na kupewa nafasi ya kueleza changamoto zake. Wazazi wajenge urafiki na watoto wao ili waweze kuwasaidia kwa karibu zaidi,” amesema.

Kwa upande wake, Mratibu wa Maendeleo ya Mtoto wa Halmashauri ya Manispaa ya Temeke, Sweetbertha Pascal, amesema halmashauri imeendelea kutoa elimu ya malezi bora na kupinga ukatili wa kijinsia katika shule na mitaa yote 42 ya manispaa hiyo.

Watoto walioshiriki maadhimisho hayo pia wamesema elimu waliyoipata imewasaidia kuelewa haki zao na namna ya kujilinda.

“Sasa tunajua umuhimu wa kutoa taarifa tunapoona au kufanyiwa vitendo visivyofaa ili tupate msaada kwa wakati,” amesema Edwin John kwa niaba ya wanafunzi.

Maadhimisho hayo yalishirikisha shule sita, walimu, viongozi wa serikali na wadau wa maendeleo ya watoto, yakibeba kaulimbiu isemayo “Mtoto ni Malezi, Msingi wa Familia Bora kwa Taifa Imara.”








Top News