Na. Saidina Msangi, WF, Dar es Salaam.

Serikali imezindua Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), hatua inayotarajiwa kuimarisha uwazi wa soko la fedha, kuongeza ufanisi wa maamuzi ya uwekezaji na kuvutia mitaji ya ndani na nje ya nchi.

Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania Bw. Emmanuel Tutuba, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amezindua Kielelezo hicho katika hafla iliyofanyika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.

Bw. Tutuba alisema kupitia Kielelezo hicho wawekezaji wataweza kuona na kufuatilia mwenendo wa faida halisi katika soko la upili la Dhamana za Serikali, jambo litakalowasaidia kufanya maamuzi ya uwekezaji kwa kuzingatia taarifa sahihi na zinazoaminika.

‘‘Kielelezo hicho kitawawezesha wawekezaji wa ndani na wa kimataifa kulinganisha viwango vya faida vya Dhamana za Serikali ya Tanzania na fursa nyingine za uwekezaji ndani ya nchi, pamoja na masoko ya kikanda na kimataifa, hivyo kuongeza uwazi wa soko, kuvutia wawekezaji wa kigeni na kuimarisha ushindani wa soko la fedha nchini’’, alisema Bw. Tutuba.

Aidha Bw. Tutuba alisema Kielelezo hicho pia kitaakisi matarajio ya soko kuhusu ukuaji wa uchumi, mfumuko wa bei na mwelekeo wa sera ya fedha, hivyo kitakuwa nyenzo muhimu kwa Benki Kuu katika kuimarisha utekelezaji wa sera ya fedha inayotegemea viwango vya riba.

‘‘Soko letu limeshuhudia ukuaji mkubwa katika kipindi cha miaka 25, ambapo mwaka 2001, Dhamana za Serikali ambazo zilikuwa hazijaiva zilifikia shilingi bilioni 499, na kuongezeka mpaka kufikia shillingi trilioni 32.3 hivi sasa’’, alisema Bw. Tutuba.

Vilevile, alisema uthaminishaji wa Dhamana za Serikali zinazowasilishwa na mabenki ya biashara kama dhamana ya kupata mikopo kutoka Benki Kuu utafanyika kwa kutumia kielelezo hicho, hatua inayotarajiwa kuongeza usahihi na uwazi katika shughuli za kifedha.

‘‘Kwa upande wa sekta ya fedha, mabenki, mifuko ya hifadhi ya jamii, makampuni pamoja na wawekezaji binafsi watanufaika kwa kutumia taarifa za kielelezo hicho kama kiwango salama cha rejea katika kupanga viwango vya riba vya mikopo, mikopo ya nyumba, hatifungani za makampuni na bidhaa nyingine za uwekezaji’’, alifafanua Bw. Tutuba.

Bw. Tutuba aliwashukuru wadau wote wa soko kwa ushiriki wao ambao umeiwezesha Serikali kupata fedha za kutekeleza miradi ya maendeleo kupitia Dhamana za Serikali pamoja na kuanza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya 2050.

Alisisitiza kuwa kuna umuhimu wa Benki Kuu na Serikali kwa ujumla kuendelea kutoa elimu ya uwekezaji ili kuhakikisha soko linaendelea kukua kwa kasi na kuongeza idadi ya wawekezaji kutoka 32,631 walioko sasa kwani idadi hiyo ni ndogo ikilinganishwa na idadi ya watu nchini.

Awali, akizungumza katika tukio hilo, Kamishna wa Idara ya Usimamizi wa Madeni, Wizara ya Fedha, Bw. Japhet Justine, alisema kuwa soko la hisa limeendelea kukua ambapo
katika mwaka wa fedha 2025/26, thamani ya miamala iliyofanyika ilikuwa zaidi ya shilingi trilioni 6.7.

Alisema soko hilo ni fursa muhimu katika kuelekea utekelezaji wa Dira 2050 ambayo sehemu kubwa ya utekelezaji wake inatarajiwa itokane na sekta binafsi kwa takribani asilimia 70 hususani katika upatikanaji wa kitaji.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), Bw. Peter Nalitolela, alisema kuwa Kielelezo hicho kitaongeza miamala na ukwasi katika soko la dhamana na kuchochea maendeleo ya aina nyingine za mali zinazouzwa katika soko la hisa.

Alipongeza Benki Kuu ya Tanzania kwa kuchapisha Kanuni za Marekebisho ya Udhibiti wa Fedha za Kigeni za mwaka 2026 na uzinduzi wa Kielelezo hicho kuwa hatua hiyo itaimarisha zaidi mfumo wa fedha nchini na kuweka mazingira yatakayowezesha Tanzania kuwa na soko la mitaji lenye ufanisi, uwazi na ushindani.

Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akibonyeza kitufe kuashiria uzinduzi rasmi wa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), katika hafla iliyofanyika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam. Wanaoshuhudia ni Kamishna Idara ya Usimamizi wa Madeni, Wizara ya Fedha, Bw. Japhet Justine (wa tatu kushoto), Naibu Gavana, Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Dkt. Yamungu Kayandabila (wa pili kushoto) na Kaimu Kamishna wa Idara ya Uendelezaji wa  Sekta ya Fedha, Wizara ya Fedha Bi. Dionisia Mjema. Kulia ni Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), Nicodemas Mkama.


Meza kuu ikiongozwa na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), wakifurahia baada ya kuzinduliwa rasmi kwa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), katika hafla iliyofanyika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.

Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akizungumnza katika hafla ya uzinduzi wa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.

Kamishna Idara ya Usimamizi wa Madeni, Wizara ya Fedha Bw. Japhet Justine, akizungumnza katika hafla ya uzinduzi wa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.

Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), Bw. Nicodemas Mkama, akizungumnza katika hafla ya uzinduzi wa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi Mtendaji wa Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), Bw. Peter Nalitolela, akizungumnza katika hafla ya uzinduzi wa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.

Baadhi ya washiriki wakifuatilia hotuba ya mgeni rasmi katika hafla ya uzinduzi wa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.

Meza kuu ikiongozwa na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba, (Katikati, walioketi), wakiwa katika picha ya pamoja na wadau baada ya kuzinduliwa rasmi kwa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), katika hafla iliyofanyika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Dar es Salaam.)




Na Janeth Raphael -MichuziTv

Tanzania imeendelea kuimarisha hadhi yake katika sekta ya mbegu barani Afrika baada ya kushika nafasi ya tatu kati ya nchi 55 kwa ubora wa mifumo ya mbegu, huku juhudi za kudhibiti mbegu feki na zisizokidhi viwango zikiongezwa ili kulinda maslahi ya wakulima na kuhakikisha usalama wa chakula nchini.

Mafanikio hayo yameelezwa na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kudhibiti Ubora wa Mbegu Tanzania (TOSCI), Nyasebwa Chimangu, ambaye amesema hatua mbalimbali zilizochukuliwa katika usimamizi wa ubora wa mbegu zimeifanya Tanzania kuendelea kuwa mfano katika bara la Afrika.

Kwa mujibu wa Chimangu, mafanikio hayo yametokana na kuimarishwa kwa ukaguzi wa mara kwa mara katika maduka ya mbegu, maghala ya kuhifadhi pamoja na viwanda vya kuchakata mbegu, kwa kushirikiana na Ofisi za Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya na vyombo vya ulinzi na usalama.

Amesema katika mwaka wa fedha 2025/2026, jumla ya watu na taasisi 22 zilizobainika kukiuka Sheria ya Mbegu zilichukuliwa hatua za kisheria, ikiwemo kufikishwa mahakamani, kutozwa faini na kuwalipa fidia wakulima waliopata hasara kutokana na matumizi ya mbegu zisizokidhi viwango.

"Tanzania imepata alama 7.25 kati ya 10 katika tathmini ya The African Seed Access Index (TASAI) ya mwaka 2023 na kushika nafasi ya tatu barani Afrika, nyuma ya Afrika Kusini iliyopata alama 8.62 na Zambia yenye alama 7.89," amesema Chimangu.

Amefafanua kuwa nafasi hiyo imechangiwa na kuimarika kwa sheria na sera za mbegu, ubora wa vifungashio, mfumo wa usajili wa aina mpya za mbegu, maendeleo ya mifumo ya mbegu inayosimamiwa na wakulima pamoja na kukua kwa biashara ya mbegu ndani na nje ya Tanzania.

Mbali na mafanikio hayo, Tanzania imeendelea kudumisha ithibati ya kimataifa ya International Seed Testing Association (ISTA), na kuifanya kuwa miongoni mwa nchi 14 za Afrika na 80 duniani zenye maabara zilizoidhinishwa kufanya upimaji wa ubora wa mbegu kwa viwango vya kimataifa.

Chimangu amesema ithibati hiyo imeipa TOSCI uwezo wa kutoa vyeti vya ISTA Orange International Certificate (OIC) kwa mbegu zinazouzwa katika masoko ya kimataifa, hatua ambayo imeongeza imani ya wawekezaji na kuvutia kampuni za kimataifa za uzalishaji na biashara ya mbegu, ambazo sasa zimefikia takribani 29 nchini.

Aidha, amesema Tanzania inaendelea kuwa mwanachama wa Skimu za Mbegu za Shirika la OECD, ikiwa ni miongoni mwa nchi 10 pekee za Afrika zinazoshiriki katika mfumo huo wa kimataifa, jambo linaloongeza ushindani wa mbegu zinazozalishwa nchini na kufungua masoko mapya ya kimataifa.

Katika mwaka wa fedha 2025/2026 pekee, TOSCI ilitoa vibali 392 vya kusafirisha nje ya nchi tani 993.21 za mbegu. Kati ya kiasi hicho, tani 722.20 zilikuwa mbegu za mikunde, tani 204.07 za nafaka, tani 55.44 za mazao ya bustani na tani 11.50 za mazao ya mafuta, takwimu zinazoonyesha kuendelea kukua kwa uzalishaji na biashara ya mbegu za Tanzania katika soko la dunia.

Hatua hizo zinaendelea kuiweka Tanzania katika nafasi nzuri ya kuwa kitovu cha uzalishaji na usambazaji wa mbegu bora barani Afrika, huku zikichochea ongezeko la tija kwa wakulima na kuimarisha mchango wa sekta ya kilimo katika uchumi wa Taifa.





Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza wakati wa uzinduzi wa Tume ya Rais ya Uchunguzi wa Wahusika wa Ghasia na Ukiukwaji wa Sheria katika Matukio ya Ghasia wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 2025, Ikulu, Jijini Dar es Salaam, tarehe 07 Agosti, 2026.












Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Wajumbe wa Tume ya Rais ya Uchunguzi wa Wahusika wa Ghasia na Ukiukwaji wa Sheria katika Matukio ya Ghasia wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 2025 mara baada ya uzinduzi wa Tume hiyo, Ikulu, Jijini Dar es Salaam, tarehe 07 Agosti, 2026.




Na Mwandishi Wetu


CHAMA cha Mawakala wa Forodha Tanzania (TAFFA) wamekuja na Mfumo wa Tanzania Customs Agent Management System (T-CAMS) unaoshirikisha TRA ikiwa ni sehemu ya mageuzi ya kidigitali yanayojenga uwazi, ufanisi na ushindani katika sekta ya uwakala wa forodha nchini.

Taarifa iliyotolewa na TAFFA kwa vyombo vya habari leo Agosti 7,2026 imesema mfumo huo unalenga kuleta uwazi katika malipo, kulinda heshima na maslahi ya mawakala wa forodha, kurahisisha huduma kwa waagizaji wa mizigo na kuongeza ufanisi wa ukusanyaji wa mapato ya Serikali.

Imeongeza kwamba mfumo huo pia ni utekelezaji wa tangazo katika gazeti la serikali (GN) namba 83 la Machi, 2026 lililotolewa na shirika la uwakala wa meli Tanzania (TASAC).

Kuhusu changamoto zilizokuwepo TAFFA imesema kwa miaka mingi, sekta ya uwakala wa forodha ilikabiliwa na changamoto kadhaa. “Kwanza, kulikuwa na migogoro ya malipo kati ya mawakala na waagizaji wa mizigo. Mara nyingi wakala alikamilisha kazi lakini malipo yalicheleweshwa au hayakulipwa kabisa.

“Pili, kulikuwepo ushindani usio wa haki ambapo baadhi ya mawakala walishusha gharama za huduma kwa kiwango kisichoendana na ubora wa kazi ili kupata wateja.Tatu, mfumo usio rasmi wa malipo uliifanya Serikali kushindwa kupata taswira sahihi ya mapato yanayotokana na sekta hii, jambo lililofungua mianya ya ukwepaji wa kodi na kupunguza uwazi.”

Kuhusu T-CAMS ni mfumo wa kidijitali unaounganisha malipo ya kodi za forodha na ada ya wakala katika utaratibu mmoja ulio wazi na unaofuatilika.

Kupitia mfumo huu, mteja analipa kwa utaratibu rasmi, ambapo kodi za Serikali na ada ya wakala zinashughulikiwa kwa uwazi. Hii inapunguza migogoro ya malipo na kuongeza uaminifu katika mnyororo mzima wa biashara.

Kwa upande wa faida kwa mawakala wa Forodha ni kwamba mfumo huo unaleta mabadiliko makubwa kwa mawakala wa forodha. Kwanza, unahakikisha wakala analipwa kwa wakati, hivyo kupunguza madeni na migogoro iliyokuwa ikiathiri biashara zao.

Pili, unajenga mazingira ya ushindani wa haki. Badala ya kushindana kwa kushusha bei kupita kiasi, mawakala watashindana kwa ubora wa huduma, utaalamu na matumizi ya teknolojia.

Tatu, historia ya mapato inayopatikana kupitia mfumo inaweza kuongeza uwezo wa mawakala kupata mikopo, kuvutia wawekezaji na kupanua biashara zao.

Nne, taaluma ya uwakala wa forodha inapata hadhi zaidi kwa kuwa huduma zake zinasimamiwa kupitia mfumo rasmi unaotambulika.

Kwa upande wa faida kwa Waagizaji wa Mizigo watanufaika kwa kupata mfumo wenye uwazi na unaotabirika na kuongeza watakuwa na uelewa wa gharama wanazopaswa kulipa kabla ya huduma kukamilika, jambo litakalowasaidia kupanga bajeti na kupunguza migogoro.

“Aidha, kwa kuwa malipo ya wakala yanahakikishwa kupitia mfumo, huduma za utoaji wa mizigo zitafanyika kwa ufanisi zaidi na kwa muda mfupi.Hali hii itapunguza gharama za ucheleweshaji wa mizigo bandarini na kuongeza ushindani wa wafanyabiashara wa Tanzania katika soko la kikanda na kimataifa.

TAFFA imesema kwa Serikali, T-CAMS ni nyenzo muhimu ya kuongeza mapato na kuboresha usimamizi wa sekta. Mfumo unarahisisha ufuatiliaji wa miamala, unapunguza mianya ya ukwepaji kodi na unatoa takwimu sahihi kwa ajili ya kupanga sera na kuboresha huduma.

Aidha, uwazi wa miamala utaongeza uaminifu wa wawekezaji na taasisi za fedha katika mazingira ya biashara nchini.

Pia kuimarishwa ushindani wa Bandari za Tanzania Bandari za Tanzania zinashindana na bandari nyingine katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini. Mbali na miundombinu bora, ushindani huo unategemea pia kasi ya utoaji wa huduma na urahisi wa kufanya biashara.

“T-CAMS ni zaidi ya mfumo wa malipo. Ni mageuzi yanayolenga kujenga sekta ya uwakala wa forodha yenye uwazi, ushindani wa haki na ufanisi mkubwa.Kwa mawakala wa forodha, mfumo huu ni kinga ya malipo na daraja la kukuza biashara zao.

“Kwa waagizaji wa mizigo, ni njia ya kupata huduma bora na za uhakika. Kwa Serikali, ni nyenzo ya kuongeza mapato, kuimarisha usimamizi na kukuza biashara,”imesema taarifa ya TAFFA.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Alhaj Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesisitiza umuhimu wa madrasa kuendelea kutoa elimu bora ya dini, sambamba na kuwajengea watoto uelewa wa mafundisho wanayopokea, maadili mema na misingi sahihi ya maisha ya Kiislamu.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 07 Agosti 2026, alipojumuika na waumini wa Dini ya Kiislamu katika Sala ya Ijumaa iliyosaliwa katika Msikiti Al Aqswaa uliopo Kiboje, Wilaya ya Kati, Mkoa wa Kusini Unguja.

Amesema elimu ya madrasa ina nafasi kubwa katika kumjenga mtoto kielimu, kiimani na kimaadili, hivyo ni muhimu watoto wasifundishwe kusoma pekee, bali waelekezwe pia kuelewa maana na tafsiri ya mafundisho wanayojifunza.

Aidha, ameeleza umuhimu wa kuendelea kuwaandaa na kuwaendeleza walimu wa madrasa ili wawe na uwezo wa kufundisha kwa ufanisi na kuwajengea watoto uelewa mpana wa elimu ya dini wanayopokea.

Halikadhalika, Rais Dkt.Mwinyi ametoa wito kwa Serikali, viongozi wa dini, wazazi na jamii kwa ujumla kuendelea kushirikiana katika kuimarisha elimu ya madrasa na kushughulikia changamoto zinazokabili taasisi hizo.

Wakati huo huo, Rais Dkt. Mwinyi amefungua rasmi Madrasa ya Fatma, iliyopo Kiboje Mkwajuni, na kueleza matumaini yake ya kuona madrasa hiyo ikitoa mchango mkubwa katika elimu na malezi ya watoto.













-Vijana na wanawake wapewa kipaumbele kunufaika na mnyororo wa thamani wa madini

Serikali kupitia Tume ya Madini imefungua fursa za biashara zenye thamani ya mabilioni ya fedha katika migodi kwa Watanzania, huku vijana na wanawake wakipewa kipaumbele ili kuongeza ushiriki wao katika Sekta ya Madini na kuchochea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Hatua hiyo inalenga kujenga uchumi shindani na jumuishi unaowezesha Watanzania kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji, kuongeza thamani ya rasilimali za madini na kunufaika zaidi na fursa zinazotokana na sekta hiyo.

Akizungumza katika Maonesho ya Nane Nane yanayoendelea katika Viwanja vya Nzuguni, Dodoma, Mjiolojia kutoka Kurugenzi ya Ukaguzi na Biashara ya Madini ya Tume ya Madini, Hassan Mkumba, amesema Tume imeainisha bidhaa na huduma 20 zitakazotolewa mahsusi na Watanzania ili kuongeza ushiriki wao katika shughuli za migodi.

Amezitaja baadhi ya huduma hizo kuwa ni usambazaji wa vilainishi migodini, huduma za usafi, huduma za kisheria zinazohusu sekta ya madini, usambazaji wa kemikali za uchenjuaji, activated carbon, uchimbaji mdogo, uchorongaji, uchambuzi wa maabara za madini, usafirishaji wa madini na huduma za ulinzi migodini.

Mkumba amesema fursa nyingine ni usambazaji wa vifaa vya usalama binafsi (PPE), uhandisi wa mitambo ya madini, matengenezo ya vifaa, usambazaji wa mafuta, upimaji na uchoraji ramani, huduma za ushauri wa kitaalamu pamoja na huduma za upishi na malazi kwa wafanyakazi wa migodini.

Amesema hatua hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa sera za Serikali za kuimarisha ushiriki wa wazawa katika mnyororo mzima wa thamani wa madini, kuongeza ajira, kukuza biashara za ndani na kuhakikisha rasilimali za madini zinachangia kwa kiwango kikubwa zaidi katika maendeleo ya uchumi wa Taifa.

Mkumba amewataka vijana, wanawake na wafanyabiashara wa Kitanzania kujitokeza na kutumia fursa hizo kwa kuzingatia viwango na mahitaji ya sekta, akisisitiza kuwa ushiriki wao utachangia kujenga uchumi imara na kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.






Na Oscar Assenga,TANGA

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Dk. Batilda Burian, ametaka elimu ya kupinga rushwa ianze kutolewa kwa wanafunzi wa shule za msingi wakiwa na umri mdogo ili kuwajengea maadili ya uadilifu, uaminifu, uwajibikaji, uzalendo na kuipenda nchi yao.

Dk. Burian alitoa kauli hiyo Agosti 6, 2026, wakati wa fainali ya shindano la Chemsha Bongo Zuia Rushwa 2026 mkoani Tanga, lililofanyika katika Shule ya Ufundi Tanga (Tanga Technical Secondary School).


Alisema kuwafundisha wanafunzi masuala ya rushwa kuanzia wakiwa darasa la tatu kutawajengea msingi imara wa kuchukia na kukemea vitendo vya rushwa, hivyo kuwa sehemu ya maisha yao ya kila siku.

Alisema wanafunzi tayari wanaonesha uelewa mkubwa kuhusu madhara ya rushwa kwa maendeleo ya taifa.


“Kama mlivyowasikia wanafunzi wakijieleza, wameonesha namna rushwa inavyodumaza maendeleo. Inaweza kusababisha kujengwa kwa madaraja mabovu kwa sababu ya kumpa kazi mkandarasi asiye na sifa. Mwisho serikali hudhani imetekeleza maendeleo, kumbe ni maendeleo ya magumashi,” alisema.
Dk. Burian, ambaye aliwakilishwa na Ofisa Elimu wa Mkoa wa Tanga, Emanuel Kisongo, alisema walimu wanapaswa kuwa mfano wa kuigwa kwa wanafunzi kwa kuwalea katika misingi ya maadili mema na kuwafundisha athari za rushwa kwa jamii na taifa.

Kwa upande wake, Kamanda wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Tanga, Ramadhan Ndwata, alisema shindano la Chemsha Bongo Zuia Rushwa 2026 linalenga kujenga kizazi chenye uadilifu kupitia wanafunzi wa shule za msingi.

Alisema maadili yanayojengwa kwa watoto yatawasaidia kukua wakiwa raia wanaochukia rushwa na kuzingatia misingi ya haki na uwajibikaji.


“Tunataka kujenga kizazi kitakachokuwa sehemu ya suluhisho la tatizo la rushwa badala ya kuwa sehemu ya tatizo. Vitendo vina nguvu kubwa katika kujenga maadili kuliko maneno pekee,” alisema.

Ndwata alisema kuanzishwa kwa klabu za wapinga rushwa katika shule za msingi kumeongeza uelewa wa wanafunzi kuhusu masuala ya rushwa.



Alisema wakati wa mashindano hayo wanafunzi walikuwa wakisahihishana wenyewe kuhusu masuala yanayohusu rushwa, jambo alilosema ni ishara ya mafanikio ya programu hiyo na kwamba wako tayari kuwaelimisha wengine.


Aidha, aliwataka wazazi kushiriki kikamilifu katika malezi ya watoto kwa kushirikiana na wadau mbalimbali kuendeleza elimu dhidi ya rushwa, akisema familia ina nafasi kubwa katika kujenga maadili ya kizazi kijacho.



Mratibu wa mashindano hayo Frank Mapunda alisema Shule ya Msingi Kombezi iliibuka mshindi wa kwanza na kujinyakulia kombe kubwa pamoja na fedha taslimu Sh200,000.



Alisema mshindi wa pili alikuwa Klabu ya Wapinga Rushwa ya Shule ya Msingi Bombo iliyopata kombe dogo na Sh150,000, huku Shule ya Msingi Chumbageni ikishika nafasi ya tatu na kujishindia ngao ya glasi pamoja na Sh100,000.



Nafasi ya nne ilichukuliwa na Klabu ya Wapinga Rushwa ya Shule ya Msingi Nguvumali iliyopata ngao ya plastiki pamoja na Sh50,000.

Mwalimu wa Shule ya Msingi Mkwakwani Faraja Mwagike alisema kuanzishwa kwa klabu za wapinga rushwa kumewaongezea wanafunzi uadilifu, ujasiri na kuwajengea msingi wa kuwa raia wema watakaoheshimu sheria na kutenda haki.



Naye mwanafunzi wa Shule ya Msingi Kisosora, Mariam Juma, alisema klabu hizo zimechangia kuwaelimisha wanafunzi kuhusu madhara ya rushwa kwa jamii na taifa.

“Ni muhimu wigo wa klabu hizi ukaongezwa ili wanafunzi wengi zaidi wanufaike na elimu hii na ujumbe uwafikie wote,” alisema.





Top News