Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imesema jumla ya malalamiko 549
(Administrative Reviews) yamewasilishwa na kushughulikiwa na Taasisi Nunuzi kupitia Moduli jambo linaloonyesha mwitikio chanya kutoka kwa wazabuni na Taasisi Nunuzi katika kutumia mfumo kwa ajili ya kupokea, kuchambua na kutoa maamuzi kuhusu malalamiko yanayohusu michakato ya ununuzi wa Umma.

Jumla ya rufaa 26 zimewasilishwa na kushughulikiwa na Mamlaka ya Rufani kupitia moduli hiyo, hatua ambayo imeongeza ufanisi katika usimamizi wa rufaa, kupunguza muda wa kushughulikia mashauri, na kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika utoaji wa haki.

James Sando Katibu Mtendaji Mamlaka ya Rufani ya Wazabuni za Umma (PPAA) ameyabainisha hayo leo jijini Dodoma katika Makutano na Waandishi wa Habari akitangaza miradi ya maendeleo na fursa za vijana kwa mwaka 2025/20.

Sando amesema kwa ujumla, takwimu hizo zinaonesha mafanikio makubwa ya awali katika matumizi ya Moduli ya kushugulikia Malalamiko na Rufaa, zinaimarisha mifumo ya ununuzi wa umma nchini kwa kuhakikisha uwazi, uwajibikaji na ufanisi katika mchakato wa Ununuzi.

Katika kuendeleza azma ya Serikali ya kuimarisha uwazi, uwajibikaji, na ufanisi katika sekta ya ununuzi wa umma hususan ushughulikiwaji wa malalamiko na rufaa zinazotokana na michakato ya ununuzi wa umma,

Mamlaka ya Rufani kwa kushirikiana na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), imekamilisha ujenzi wa Moduli ya Kupokea na kushughulikia Malalamiko na Rufaa zinazotokana na michakato ya Ununuzi wa Umma (Complaints and Appeals Management Module).

"Moduli hii ipo katika Mfumo wa Ununuzi wa Umma kwa Njia ya Kielektroniki (NeST), na inatoa njia rahisi, ya haraka, na yenye uwazi kwa wadau wote kushiriki katika mchakato wa usulushi wa migogoro ya ununuzi"

Amesema inachangia kwa kiasi kikubwa kuboresha utendaji na kuimarisha imani katika mfumo wa ununuzi wa umma.

Hata hivyo Sando amesema Serikali kupitia Wizara ya Fedha ilizindua rasmi matumizi ya moduli hiyo Februari 2025, Tangu uzinduzi huo, moduli imeleta mageuzi chanya katika namna taasisi za umma zinavyoshirikiana na Mamlaka ya Rufani kupokea, kusajili na kushughulikia malalamiko na rufaa kutoka kwa wazabuni walioshiriki katika michakato ya ununuzi wa umma na kwa sasa, malalamiko yote yanawasilishwa kupitia moduli ya Usimamizi wa Malalamiko na Rufaa katika mfumo wa NeST.

"Moduli hii imeendelea kutumika na wadau mbalimbali kwa madhumuni ya kuwasilisha na kushughulikia malalamiko na rufaa kwa njia ya kielektroniki, ikileta ufanisi mkubwa katika mchakato mzima.

Sando atoa wito kwa wazabuni wote nchini pamoja na wadau wa ununuzi wa umma kushiriki mafunzo ya matumizi ya moduli hiyo pale Mamlaka ya Rufani inapoyatangaza Mafunzo.

yatawawezesha kuelewa namna bora ya kutumia moduli hiyo pale wanapokabiliwa na changamoto katika michakato ya ununuzi wa umma.




Na Pamela Mollel, Arusha

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mwigulu Nchemba, ameonyesha kuridhishwa na mwenendo wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayoendelea katika Jiji la Arusha, akisema kasi iliyopo inaleta matumaini mapya kwa wananchi.

Katika ziara yake ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa stendi kuu ya mabasi katika eneo la Bondeni City,Waziri Mkuu alisisitiza umuhimu wa miundombinu bora itakayokidhi mahitaji ya ukuaji wa jiji hilo. Alielekeza pia ujenzi wa barabara za njia nne ili kupunguza msongamano wa magari, sambamba na kuhimiza matumizi ya mabasi ya mwendokasi yanayotumia nishati safi ikiwemo gesi na umeme.

Akizungumza na wananchi na viongozi wa eneo hilo, Dkt. Nchemba alisema utekelezaji wa miradi hiyo ni sehemu ya dhamira ya Serikali katika kuimarisha huduma za kijamii na kukuza uchumi wa taifa. 

Alibainisha mafanikio yaliyopatikana katika sekta mbalimbali zikiwemo afya, elimu na nishati, akitolea mfano ujenzi wa hospitali za wilaya, vituo vya afya na zahanati pamoja na upatikanaji wa vifaa tiba vya kisasa katika hospitali za rufaa na mikoa.

Aidha, aliwataka wakandarasi waliolipwa na Serikali kuhakikisha wanalipa wafanyakazi wao kwa wakati, akionya kuwa haki za wafanyakazi zinapaswa kulindwa. Kuhusu vizimba vya wafanyabiashara katika stendi hiyo, alisisitiza vitolewe kwa walengwa halisi wanaofanya biashara badala ya kuhodhiwa kwa lengo la kupangisha kwa bei ya juu.

Katika ziara hiyo, Waziri Mkuu alipokea na kutatua baadhi ya kero za wananchi, akiahidi kuendeleza utaratibu huo katika maeneo mengine nchini.

Kwa upande wake, Waziri wa Habari, Michezo, Sanaa na Utamaduni, Paul Makonda, alimpongeza Waziri Mkuu kwa msisitizo wake wa kusikiliza changamoto za wananchi na kuzitafutia suluhisho. Alieleza kuwa Arusha kuna jumla ya miradi 52 inayoendelea kutekelezwa kwa kuzingatia Ilani ya Chama Cha Mapinduzi.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Amos Makalla, aliwahimiza wakandarasi kuongeza bidii ili kuhakikisha miradi inakamilika kwa wakati. Aliahidi ushirikiano wa karibu kati ya ofisi yake na wadau mbalimbali ili kusimamia utekelezaji wa miradi hiyo.

Hata hivyo, alionya dhidi ya migogoro isiyo ya lazima kati ya wafanyabiashara na baadhi ya watumishi wasio waadilifu, akisisitiza umuhimu wa uwajibikaji na maadili katika utekelezaji wa majukumu ya umma.





Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe Adolph Mkenda afungua mlango wa mazungumzo kwa Taasisi na Makampuni mbalimbali kuunga mkono juhudi za Rais Dkt Samia kusomesha Wanafunzi wanaofanya vizuri katika masomo ya Sayansi kutoka ngazi ya awali ya kidato cha sita hadi ngazi ya Shahada ya Uzamili kwani Wizara imejipanga vizuri kuhakikisha fedha watakazotoa zinakwenda mahali panapotakiwa

Waziri Mkenda ameyasema hayo leo Jijini Dodoma Februari 25,2026 wakati akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu kutolewa kwa ufadhili huo na Wanafunzi kuripoti katika Vyuo husika.

Ambapo amesema kuwa tayari walishapanga kutoa ufadhili katika ngazi ya Shahada ya Uzamili na kwa kuanza waliamua kupeleka Wanafunzi katika Vyuo viwili vya hapa nchini cha Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Arusha na kampasi ya Indian Institute of Teknoloji kilichopo Zanzibar ambavyo vyote vimejikita katika masuala ya Sayansi. 

Na kuongeza kuwa tayari Wanafunzi wamesharipoti katika Chuo cha Nelson Mandela na kuanza masomo kwa ngazi ya Shahada ya Uzamili na kwa awamu ya pili watawapeleka wengine tena 10 katika kampasi ya Indian Institute of Teknoloji kwaajili ya kusoma  mambo ya Data Science,Akili unde na mambo mengine ya kisayansi ili kuendana na kasi ya Dunia katika Sayansi na Teknolojia. 

"Kwahiyo napenda nitoe kauli hii kwa Benki,Migodi,Taasisi na Mashirika mbalimbali ambayo yanapenda kuunga mkono juhudi za Rais wetu za kusomesha tukae tuongee na tutakuwa na mkutano wa kuzungumza pamoja na kuwahakikishia tutakavyogawa nafasi bila bila kona kona ili hela mtakazoleta ziende mahali panapotakiwa".

Aidha amesema kuwa kwa mwaka huu wameanza kutekeleza maelekezo ya Serikali kwa kupeleka vijana waliofanya vizuri kwenda kusoma masuala ya Data Science, Akili unde na mambo mengine ya kisayansi ambapo tayari wameshapeleka wanafunzi 16 huko Johannesburg Afrika ya Kusini na wameanza masomo kwa ufadhili huo.

Ambapo pia wanafunzi wengine 34 wanatajiwa kuondoka kati ya mwezi wa 8 au 9 kwenda Iland kwaajili ya masomo hayo hayo ya Sayansi. 

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu Tume ya Sayansi na Teknolojia ambao ndio waratibu wa Program hiyo ya Samia Scholarship Extended Dkt Amos Nungu amesema kuwa wameona muitikio mkubwa kwa watoto na thamani ambayo watoto wameipa program hiyo,na kuamini kuwa idadi itaongezeka kwa wakati mwingine, zaidi ya hawa walioenda katika awamu hii.

Naye Makamu Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Arusha ambao ndio watekelezaji wa programu hii Prof Maulilio Kipanyula amesema Taasisi hiyo haikuchaguliwa kwa bahati mbaya kwasababu Wanafunzi wanaokwenda pale wanapata kuchanganyikana na wanafunzi kutoka Mataifa mengine kwani asilimia 10 ya wanafunzi wao ni wa Kimataifa hivyo wanapata uzoefu kupitia kukutana kwao na kuwa pamoja.






 

Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Uendelezaji Miji na Vijiji kutoka TAMISEMI, Rachel Kaduma, amesema utekelezaji wa Mradi wa Green and Smart Cities unaendelea katika hatua mbalimbali ukiwa na lengo la kuboresha maisha ya wananchi, kuongeza ajira kwa vijana na kuimarisha huduma za kijamii katika maeneo ya mijini.

Akizungumza leo Februari 25, 2026 Jijini Dar es Salaam katika kikao cha tathmini ya utekelezaji wa mradi huo , Kaduma alisema mradi unahusisha ukarabati na uboreshaji wa miundombinu ya kiuchumi ikiwemo maeneo ya uvuvi, pamoja na kuwajengea uwezo vijana kupitia mafunzo ya ufundi stadi katika vyuo vya VETA.

Alifafanua kuwa mafunzo hayo yanawawezesha vijana kupata ujuzi wa kujiajiri au kuajiriwa katika sekta mbalimbali za uchumi.

“Lengo la mradi huu si tu kuboresha miundombinu, bali pia kuhakikisha miji inakuwa safi, salama na yenye mazingira rafiki kwa wananchi. Huduma muhimu zinaimarishwa ili wananchi wapate huduma bora kwa urahisi,” alisema Kaduma.

Aidha, alibainisha kuwa kikao hicho kimeandaliwa kujadili changamoto zinazojitokeza wakati wa utekelezaji wa mradi na kutoa mapendekezo yatakayowasilishwa kwa viongozi wa juu kwa ajili ya maamuzi.

“Tunapitia changamoto mbalimbali, lakini pia tunapata fursa ya kubadilishana uzoefu kati ya wadau. Wale waliofanikiwa wanashirikisha wenzao mbinu walizotumia kuboresha utekelezaji,” aliongeza.

Kwa upande wake, Mratibu wa Programu ya Green and Smart Cities katika Manispaa ya Ilemela, Ahmed Sakif, alisema programu hiyo inafadhiliwa na Umoja wa Ulaya kwa kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Alieleza kuwa mradi ulianza mwaka wa fedha 2022/2023 na unatekelezwa katika halmashauri mbalimbali zikiwemo Jiji la Mwanza na Jiji la Tanga.

Sakif alitaja maeneo makuu matatu ya utekelezaji kuwa ni msaada wa kibajeti kwa halmashauri, uboreshaji wa miundombinu ya umma kama masoko na mialo ya samaki, pamoja na uhifadhi wa mazingira na rasilimali maji.

Aliongeza kuwa kupitia mradi huo, vijana zaidi ya 600 wamepata mafunzo ya ufundi stadi na wanatarajiwa kuunganishwa na fursa za mitaji ili kuanzisha shughuli za kujiajiri.

Wadau wa mradi huo wamesema hatua zilizofikiwa zinaonesha mafanikio, huku wakisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya serikali, mashirika ya maendeleo na wananchi ili kuhakikisha mradi unaleta matokeo chanya.

Akizungumza kwa niaba ya Umoja wa Ulaya, Ulrik Jorginsen alisema ujumbe wa EU nchini Tanzania unatekeleza programu hiyo kwa kushirikiana na serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu.

Alisema programu inalenga kusaidia maendeleo endelevu katika miji ya Tanzania, hususan miji ya sekondari, kwa kuboresha huduma muhimu kama maji safi na usafi wa mazingira.

“Kazi kubwa imefanyika katika maeneo ya Unguja na Pemba, hususan katika upanuzi wa miundombinu ya maji na usafi wa mazingira,” alisema.

Aliongeza kuwa awamu zinazofuata za mradi zinaendelea, huku mipango ikiwekwa ya kuanzisha miradi kama hiyo katika Jiji la Tanga ili kuboresha huduma za msingi kadri miji inavyokua.

“Mbali na sekta ya maji, programu pia inashughulikia maendeleo ya masoko na biashara ndogo ndogo kupitia mpango wa Inclusivity,” alisisitiza.

Kupitia mpango huo, vijana na wanawake wanapewa fursa ya kuimarisha biashara zao na kuunganishwa na masoko, hatua inayolenga kukuza uchumi wa ndani na kuongeza ajira.

Jorginsen alihitimisha kwa kusisitiza kuwa ujenzi wa uwezo wa taasisi za ndani ni muhimu ili ziweze kusimamia miradi hiyo kwa uendelevu hata baada ya programu kukamilika.












NA EMMANUEL MBATILO, MICHUZI TV

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dorothy Gwajima, amesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya serikali, mashirika yasiyo ya kiserikali na wadau wa maendeleo katika kuboresha ustawi wa jamii na watoto nchini. 

Akizungumza leo Februari 25, 2026 katika uzinduzi wa mkakati wa miaka Mitano wa World Vision Tanzania uliofanyika Jijini Dar es Salaam, Waziri Gwajima alisema kuwa jitihada za pamoja zimekuwa na mchango mkubwa katika kuwafikia watoto na familia nyingi zilizo katika mazingira magumu.

Alieleza kuwa serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan imeweka kipaumbele katika kuboresha malezi, elimu, afya na ulinzi wa watoto. 

Aidha, aliipongeza World Vision Tanzania kwa kazi kubwa wanayofanya katika maeneo mbalimbali ya nchi, ikiwemo kuwajengea uwezo wanawake na vijana kiuchumi, kuimarisha ulinzi wa watoto dhidi ya ukatili, pamoja na kusaidia jamii kupata maji safi na huduma muhimu za kijamii.

Waziri Gwajima pia alibainisha kuwa mkakati mpya wa shirika hilo unalenga kuwafikia mamilioni ya watoto na kuimarisha mifumo ya kijamii inayosaidia ustawi wa jamii.

 Alisema serikali itaendelea kushirikiana na mashirika ya maendeleo ili kuhakikisha mipango hiyo inatekelezwa kwa ufanisi na kuleta matokeo chanya kwa wananchi.

Katika hotuba yake, alitoa wito kwa wadau wote, ikiwemo sekta binafsi, viongozi wa dini na wananchi, kuendelea kushiriki katika programu zinazolenga maendeleo ya watoto na familia. 

Alisisitiza kuwa uwekezaji katika ustawi wa watoto ni msingi muhimu wa kujenga rasilimali watu bora kwa maendeleo ya taifa.

Nae Mwenyekiti wa Bodi ya World Vision Tanzania, Victori Elangwa, alisema mkakati huo umejengwa juu ya imani kwamba mabadiliko ya kweli hutokea pale wadau wanapotembea pamoja kwa mshikamano na uwajibikaji wa pamoja. 

Aidha, Elangwa alieleza kuwa taasisi hiyo inaadhimisha utekelezaji wa mpango wa WASH unaoweka kipaumbele kwenye maji safi, usafi wa mazingira na nishati, akibainisha kuwa huduma hizo ni msingi wa afya bora na mafanikio ya kielimu kwa watoto. 

Alisema watoto wanapopata maji safi ya kunywa, shule na vituo vya afya vinapokuwa na mifumo bora ya maji na usafi, pamoja na jamii kujengewa uwezo wa kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi, matokeo yake huwa ni mabadiliko chanya yanayoonekana katika maisha yao.

Alitumia fursa hiyo kuishukuru Serikali ya Tanzania kwa ushirikiano na uongozi wake madhubuti, pamoja na wadau na marafiki mbalimbali wanaoamini katika uwezo wa kila mtoto. 

Elangwa alitoa wito kwa wananchi, taasisi za binafsi, mashirika na jumuiya kushiriki kikamilifu katika harakati hizo kwa kuchangia, kushirikiana na kuunga mkono dhamira ya kuhakikisha hakuna mtoto anayesalia nyuma katika safari ya maendeleo ya taifa.
























Top News