Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imewasihi wadau wa ununuzi wa umma na wananchi kwa ujumla kutembelea banda la Mamlaka ya Rufani kupata uelewa juu ya majukumu na huduma mbalimbali zinazotolewa na taasisi hiyo hususan matumizi ya Moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST.


Wito huo umetolewa na Mkuu wa Sehemu ya Huduma za Sheria PPAA, Bi. Agnes Sayi kwa niaba ya Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando. Bi Sayi alitoa wito huo leo tarehe 01 Julai, 2026 katika Banda la Wizara ya Fedha Jijini Dar es Salaam kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba). 

Pamoja na mambo mengine, PPAA katika maonesho hayo inatoa elimu kuhusu uamuzi juu ya rufaa zinazotokana na mchakato wa ununuzi wa umma, uamuzi juu ya rufaa zinazotokana na kufungiwa kushiriki katika michakato ya ununuzi wa umma pamoja na uamuzi juu ya malalamiko yanayotokana na kushindwa kwa Afisa Masuuli kutoa uamuzi ndani ya muda uliowekwa.

“Maeneo mengine yanayotolewa elimu ni uamuzi juu ya malalamiko baada ya mkataba wa ununuzi kuanza kutekelezwa, uamuzi juu ya maombi ya kuongezewa muda wa kuwasilisha rufaa nje ya muda uliowekwa, uamuzi juu ya maombi ya utekelezaji wa amri ya Mamlaka ya Rufani, uamuzi juu ya maombi ya kufuta uamuzi uliotolewa bila kusikiliza upande mwingine (Ex Parte decision) na uamuzi juu ya maombi ya kurejesha rufaa,” amesema Bi. Sayi

Maonesho hayo yameanza tarehe 28 Juni yataendelea hadi 13 Julai 2026 katika Viwanja vya Mwl. Nyerere Jijini Dar es Salaam. Aidha, Taasisi mbalimbali za Umma zimeshiriki maonesho hayo kwa lengo la kuonesha huduma wanazotoa kwa wananchi kwa kaulimbiu: Maonesho ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba, Fahari ya Tanzania.




 

 

Naibu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya EWURA, Mha. Ngosi Mwihava (kushoto) na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Ndg. Gerald Maganga (Kulia) wakimkabidhi Mh. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan mfano wa hundi kama ishara ya kukabidhi Hazina mchango wa kisheria wa taasisi hiyo wa Sh. 10.6 bilioni, kwa mwaka wa Fedha 2025/26, kwenye hafla iliyofanyika Ikulu jana.

 
Na FARIDA MANGUBE MOROGOGO


Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima, amesema kada ya Maendeleo ya Jamii inapaswa kuwa injini ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwa kuongoza mageuzi ya fikra, kuimarisha uchumi wa wananchi na kujenga jamii yenye maarifa, uzalishaji, ubunifu na uzalendo.

Ameyasema hayo Leo Julai 1 Mjini Morogoro wakati akifungua kikao kazi cha Wakuu wa Vitengo vya Maendeleo ya Jamii ngazi ya mikoa, Dkt. Gwajima amesema mafanikio ya Dira ya 2050 hayatategemea ukubwa wa bajeti au idadi ya miradi ya maendeleo, bali uwezo wa kubadilisha fikra na tabia za Watanzania katika kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya Taifa.

Waziri Gwajima amewataka wakuu wa vitengo vya maendeleo ya jamii kuhamasisha mapinduzi ya fikra yatakayojenga utamaduni wa kuthamini kazi, uzalishaji, ubunifu, matumizi ya teknolojia, uwajibikaji na kujitegemea. Aidha, alisema ni wakati wa kuifanya taaluma ya maendeleo ya jamii itumie mifumo ya kidijitali na taarifa zinazotokana na ushahidi ili kupanga na kutekeleza afua zenye matokeo yanayopimika kwa wananchi.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Eliakim Maswi, amesema utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 unahitaji mabadiliko makubwa katika sekta ya maendeleo ya jamii ili iweze kutekeleza wajibu wake kwa ufanisi.

Ameeleza kuwa pamoja na Serikali kuendelea kuwekeza katika miradi mikubwa ya maendeleo, mafanikio yake yatategemea pia mabadiliko ya wananchi kupitia kazi ya maafisa wa maendeleo ya jamii.

Naye Mwenyekiti wa Wakuu wa Vitengo vya Maendeleo ya Jamii Tanzania Bara, Elis Simonile, amesema kikao hicho kimewapa fursa ya kujitathmini, kubaini changamoto na vikwazo vinavyoikabili kada hiyo pamoja na kuweka mikakati ya kuboresha utendaji kwa lengo la kuleta mabadiliko ya tabia na kuimarisha uzalendo miongoni mwa wananchi.

Simonile amesema vitendea kazi walivyokabidhiwa vitasaidia kuongeza ufanisi wa kazi kwa kuwa awali uhaba wa vifaa ulikuwa kikwazo kikubwa katika kuwafikia wananchi. Aliongeza kuwa matumizi ya mifumo ya kidijitali yatawezesha ukusanyaji na uchambuzi wa taarifa sahihi, hivyo kurahisisha utoaji wa ujumbe na utekelezaji wa afua za maendeleo ya jamii kwa ufanisi zaidi.

Kikao kazi hicho kilichowakutanisha Wakuu wa Vitengo vya Maendeleo ya Jamii kutoka mikoa yote ya Tanzania Bara kililenga kutathmini utekelezaji wa majukumu ya kada hiyo, kubadilishana uzoefu na kuweka mikakati ya kuimarisha mchango wake katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Kikao hicho kilihitimishwa kwa ugawaji wa vitendea kazi, ikiwemo kompyuta mpakato kwa lengo la kuimarisha matumizi ya mifumo ya kidijitali katika ukusanyaji, uchambuzi na utoaji wa taarifa za maendeleo ya jamii kwa wakati.







Standard Chartered Tanzania kwa kushirikiana na Nipe Fagio imeadhimisha miaka 20 ya programu ya kujitolea kwa jamii ya Standard Chartered duniani kwa kufanya zoezi la kila mwaka la usafi wa fukwe katika Ufukwe wa Silversand, Kunduchi.

Jumla ya washiriki 74, wakiwemo watoto 20, walishiriki katika zoezi hilo lililolenga kuchangia uhifadhi wa mazingira na kuhamasisha ushiriki wa wafanyakazi katika shughuli za maendeleo ya jamii.

Akizungumza kuhusu shughuli hiyo, Afisa Mtendaji Mkuu na Mkuu wa Kitengo cha Coverage wa Standard Chartered Bank Tanzania, Geofrey Mchangila, alisema:

"Zoezi la mwaka huu lina umuhimu wa pekee kwetu kwani linafanyika wakati Standard Chartered inaadhimisha miaka 20 ya kujitolea kwa jamii duniani kote. Tunaamini kuwa mabadiliko ya kweli huanza pale watu wanapounganisha nguvu zao. 

Kupitia ushirikiano wetu na wafanyakazi, familia zao pamoja na Nipe Fagio, tunaendelea kuchangia kulinda ukanda wa pwani wa Tanzania na kujenga jamii zenye afya bora na mazingira endelevu kwa vizazi vijavyo."

Katika zoezi hilo, washiriki walisafisha eneo lenye ukubwa wa takribani mita za mraba 4,000 za ufukwe na kukusanya kilo 506 za taka zilizohifadhiwa katika mifuko 55. 

Uchambuzi wa taka zilizokusanywa ulionyesha kuwa plastiki, hususan povu la polystyrene na chupa za plastiki za vinywaji, ndizo zilikuwa taka zilizopatikana kwa wingi, hali inayodhihirisha umuhimu wa kuendelea kuchukua hatua za kudhibiti uchafuzi wa mazingira ya bahari.

Kwa kipindi cha miaka mitatu iliyopita, kupitia ushirikiano wake na Nipe Fagio, Standard Chartered Tanzania imefanikisha jumla ya kampeni tano za usafi wa fukwe, ikihusisha washiriki 594, kusafisha zaidi ya mita za mraba 32,000 za ukanda wa pwani na kukusanya karibu tani tano za taka.

Mpango huu ni sehemu ya mkakati mpana wa Standard Chartered wa kuendeleza uhimilivu wa mazingira na maendeleo endelevu, huku ukiunga mkono Malengo ya Maendeleo Endelevu ya Umoja wa Mataifa (SDGs), hususan Lengo la 13 la Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi, Lengo la 14 la Kuhifadhi Maisha ya Chini ya Maji na Lengo la 17 la Kuimarisha Ushirikiano kwa Ajili ya Kufanikisha Malengo.

Standard Chartered inapoendelea kuadhimisha miaka 20 ya programu yake ya kujitolea kwa jamii, inaendelea kuwahamasisha wafanyakazi wake kutumia muda, ujuzi na utaalamu wao kuleta mabadiliko chanya na endelevu katika jamii na mazingira.










Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi Mteule wa Tanzania nchini Uganda, Mhe. Balozi Meja. Jen. Marco Elisha Gaguti, mazungumzo yaliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam leo tarehe 01 Julai 2026.

Mazungumzo hayo ni kufuatia, Mhe. Balozi Gaguti, kufika kwa Makamu wa Rais kwa lengo la kumuaga akielekea katika Kituo chake cha kazi nchini Uganda, mara baada ya kuteuliwa hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.








Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda akikata utepe (kulia) akikata utepe kuashiria uzinduzi wa huduma za Next Generation Sequencing (NGS) unaoashiria enzi mpya ya tiba ya jenomiki, ukikiweka Chuo Kikuu kuwa kitovu cha kitaifa na kikanda cha sayansi ya jenomiki, uchunguzi wa kisasa wa magonjwa, utafiti na ubunifu. anayeshuhudia katikati ni Makamu Mkuu wa chuo cha MUHAS, Profesa, Appolinary Kamuhabwa.

Na Karama Kenyunko Michuzi Tv 

SERIKALI imewataka wanasayansi na wataalamu wa afya kuziba pengo lililopo kati ya tiba asili na tiba ya kisasa kwa kufanya tafiti za kisayansi zitakazothibitisha usalama na ufanisi wa tiba za asili ili ziweze kuingizwa rasmi katika mfumo wa huduma za afya nchini.

Wito huo umetolewa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, wakati akifungua Mkutano wa 14 wa Kisayansi wa Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) uliofanyika leo Julai Mosi, 2026 katika kampasi ya Mloganzila jijini Dar es Salaam.

Prof. Mkenda amesema ni muhimu kubadili matumizi ya tiba za asili zinazotumiwa na wananchi kuwa tiba zinazotegemea ushahidi wa kisayansi kupitia tafiti, majaribio ya kitabibu na uthibitisho wa kitaalamu.

Amesema madai yote kuhusu ufanisi wa tiba, yakiwemo yale ya tiba za asili, yanapaswa kuthibitishwa kisayansi ili kubaini usalama wake, kiwango sahihi cha matumizi na aina ya wagonjwa wanaoweza kunufaika nazo.

“Lengo si kupinga tiba asili, bali kuziinua kupitia sayansi ili zitumike kwa usalama ndani ya mfumo wa huduma za afya,” amesema.

Aidhqla, Prof. Mkenda ameibainisha kuwa Serikali itaratibu warsha za kitaifa zitakazowakutanisha watafiti, waganga wa tiba asili, wadhibiti na wataalamu wa haki miliki ili kuweka mfumo wa kutathmini na kulinda maarifa ya tiba za asili.

Pia, ameonya kuwa kutegemea ushuhuda usiofanyiwa uthibitisho wa kisayansi kunaweza kuwaweka wagonjwa katika hatari ya kutumia tiba zisizo salama au zisizo na ufanisi, akisisitiza umuhimu wa majaribio ya kitabibu, uchunguzi wa maabara na tafiti za kina kabla ya tiba yoyote kukubalika.

Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi la MUHAS, Makata Yambi, amesema ubunifu na tafiti zinazozalishwa nchini zina nafasi muhimu katika kuimarisha mfumo wa afya, huku mkutano huo ukiwa jukwaa la watafiti, watunga sera na wadau wa maendeleo kubadilishana uzoefu na kutafuta suluhisho la kuboresha huduma za afya kwa wote.

Naye, Makamu Mkuu wa MUHAS, Prof. Appolinary Kamuhabwa, amesema chuo kinawekeza katika teknolojia za kisasa ikiwemo akili bandia (AI), genomiki na uchunguzi wa magonjwa kwa mbinu za kisasa ili kuimarisha tafiti na utoaji wa huduma za afya.
Amesema kuanzishwa kwa huduma za uchunguzi wa kizazi kipya wa vinasaba (Next Generation Sequencing) kunaifanya MUHAS kuwa kitovu cha kikanda katika sayansi ya jenomu na tiba mahsusi, hatua itakayosaidia pia kutathmini kwa kina tiba zinazotokana na maarifa ya tiba asili.

Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Mkutano wa Kisayansi wa MUHAS, Prof. Raphael Sengeja, amesema mwaka huu mkutano umepokea jumla ya tafiti 247, zikiwemo 138 za uwasilishaji wa moja kwa moja na 109 za mabango, zikihusu tiba asili, akili bandia, genomiki, afya ya uzazi, usugu wa vimelea dhidi ya dawa na uimarishaji wa mifumo ya afya.
Amesisitiza kuwa lengo la mkutano huo ni kuhakikisha tafiti zinazofanywa hazibaki kwenye machapisho ya kitaaluma pekee, bali zinatafsiriwa kuwa suluhisho halisi litakaloboresha afya na ustawi wa jamii.







Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali imeweka mkakati wa kuharakisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo nchini ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na miradi inakamilika kwa wakati.

Akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika Uwanja wa Sokoine, wilayani Serengeti, mkoani Mara, leo Jumatano (Julai 1, 2026), Waziri Mkuu alisema Serikali imeanza rasmi utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2025–2030, Bajeti ya Serikali ya mwaka 2026/2027 pamoja na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

"Tunaanza utekelezaji wa Ilani leo, Ilani ya 2025–2030. Tunaanza utekelezaji wa Bajeti leo ya mwaka 2026/2027, na tunaanza utekelezaji wa Dira mpya ya 2050 leo."

Waziri Mkuu alisema baadhi ya miradi ya maendeleo ilichelewa kuanza au kupungua kasi ya utekelezaji kutokana na uamuzi wa kimkakati wa Serikali wa kuelekeza rasilimali katika kukamilisha miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo Mradi wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere, Daraja la JPM na Reli ya Kisasa (SGR), ambayo sasa imeanza kuwanufaisha Watanzania.

Akizungumzia utekelezaji wa miradi ya barabara, Waziri Mkuu alisema Serikali imeweka utaratibu mpya utakaohakikisha fedha za Mfuko wa Barabara zinawafikia watekelezaji moja kwa moja ili kuondoa ucheleweshaji wa miradi.

"Kuanzia leo tarehe moja, fedha zitakazokusanywa zinazotakiwa kwenda kwenye ujenzi wa barabara, zikishakusanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania, hazitapelekwa kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali. Zitakwenda moja kwa moja kwenye Mfuko wa Barabara ili kasi ya ujenzi wa barabara isiende kwa kusuasua."

Alisema hatua hiyo itawawezesha wakandarasi waliokuwa wamesimama kurejea katika maeneo ya kazi na kuharakisha utekelezaji wa miradi mbalimbali ikiwemo ya Mkoa wa Mara.

"Nimewaelekeza wakandarasi ambao walishatoka site warudi site, kwa sababu kuanzia leo tarehe moja Mfuko wetu wa Barabara... fedha zitakwenda moja kwa moja kwenye mifuko ili wananchi wapate maendeleo yanayochochewa na miundombinu hiyo wezeshi."

Aidha, Waziri Mkuu aliwahakikishia wananchi kuwa Serikali itaendelea kusimamia utekelezaji wa ahadi zote zilizotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.

"Yale ambayo Mheshimiwa Rais aliwaahidi, amenituma niwahakikishie kuwa yatatekelezwa. Na mimi, kama wajibu niliopewa na Katiba, nitasimamia kuhakikisha maelekezo hayo ya Mheshimiwa Rais yanatekelezwa."








Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Jumatano, Julai 1, 2026, amekagua maendeleo ya ujenzi wa Jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti, lililopo mjini Mugumu, mkoani Mara, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi ya siku tano mkoani humo.

Akiwasilisha taarifa ya ujenzi huo, Msanifu Majengo wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) Mkoa wa Mara, Bw. Nicholas Jeje, alisema mradi huo unagharimu shilingi bilioni 4.5 zinazotolewa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Alisema ujenzi ulianza Aprili 10, 2025 na unatarajiwa kukamilika Aprili 9, 2028, huku utekelezaji wake ukiwa umefikia asilimia 42.

Alieleza kuwa jengo hilo litakuwa na ofisi 62, zikiwemo ofisi za Mkurugenzi wa Halmashauri na Mwenyekiti wa Halmashauri, pamoja na kumbi mbili za mikutano zenye uwezo wa kuchukua watu 50 na 110 mtawalia, hatua inayolenga kuboresha mazingira ya utoaji wa huduma kwa wananchi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mara, Kanali Evans Mtambi, alimkaribisha Waziri Mkuu mkoani humo na kusema ziara hiyo itamwezesha kutembelea wilaya zote sita, halmashauri zote tisa na majimbo yote 10 ya uchaguzi yaliyopo mkoani Mara, ambapo pamoja na mambo mengine atakagua miradi ya maendeleo na kuzungumza na wananchi.








 

Mwenyekiti wa Taifa Group na mfanyabiashara mashuhuri, Bw. Rostam Azizi, ametunukiwa Tuzo ya Juu ya Heshima ya Chemba ya Taifa ya Biashara Tanzania (TNCC) kwa kutambua mchango wake katika kukuza uwekezaji, kuunda ajira, kuboresha huduma za jamii na kuchochea maendeleo ya uchumi wa Taifa.

Tuzo hiyo ilikabidhiwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, aliyekuwa mgeni rasmi katika Kongamano la Biashara na Uwekezaji la Mwaka 2026 lililoandaliwa na TNCC katika Hoteli ya Johari Rotana, Dar es Salaam.

Akizungumza katika kongamano hilo, Dkt. Mwigulu alisema Serikali itaendelea kuimarisha mazingira ya biashara na uwekezaji kupitia maboresho ya sera, sheria, kanuni na mifumo ya utoaji huduma ili kuiwezesha sekta binafsi kuwa injini ya ukuaji wa uchumi na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

"Ajenda ya sekta binafsi ni ajenda ya Taifa. Hatuwezi kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 bila sekta binafsi yenye nguvu na inayoshirikiana kwa karibu na Serikali," amesema.

Aliongeza kuwa Serikali itaendelea kushughulikia mapendekezo ya sekta binafsi ili kuondoa vikwazo vya biashara na kuongeza ushindani wa bidhaa na huduma za Tanzania katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Kupitia uwekezaji wake katika sekta mbalimbali, Bw. Rostam Azizi amechangia uundaji wa maelfu ya ajira, kukuza uwekezaji na kuboresha huduma za jamii, hatua zilizochangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya uchumi wa Taifa.

Akizungumza baada ya kupokea tuzo hiyo, Bw. Rostam Azizi aliishukuru Serikali na TNCC kwa kutambua mchango wake, akisema tuzo hiyo ni motisha ya kuendelea kushiriki katika maendeleo ya Taifa.

"Ninapokea tuzo hii kwa heshima kubwa.

Naihusisha na juhudi za pamoja kati ya sekta binafsi na Serikali katika kujenga uchumi imara. Nawapongeza pia wadau wote waliotunukiwa tuzo mbalimbali leo kwa mchango wao katika kuimarisha sekta binafsi na kukuza uchumi wa Taifa," amesema.

Katika hafla hiyo, Waziri Mkuu pia alikabidhi tuzo mbalimbali kwa wadau wengine, akiwemo Bi. Emma Kawawa, Bw. David Mwaibula, Bw. Imani Kajula, Bw. Elibariki Mmasi na Bi. Mercy Emmanuel Sila, kwa mchango wao katika kuendeleza sekta binafsi, kuboresha mazingira ya biashara na kuimarisha shughuli za TNCC.

Na Mwandishi wetu Dodoma

Kampuni ya Alliance Life Assurance Ltd imeandika historia mpya katika sekta ya bima nchini baada ya kuzindua rasmi ofisi yake ya mauzo jijini Dodoma, hatua inayoiweka kama kampuni ya kwanza ya bima ya maisha kuwa na uwepo rasmi katika Makao Makuu ya nchi.

Uzinduzi huo umefanyika katika hafla iliyohudhuriwa na wadau mbalimbali wa sekta ya bima, akiwemo Meneja wa Mipango na Utafiti wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA), Edgar Shao, aliyemwakilisha Kamishna wa Bima, Dkt. Baghayo A. Saqware.

Akizungumza katika hafla hiyo, Shao aliipongeza Alliance Life Assurance kwa hatua hiyo, akibainisha kuwa ni ishara ya wazi ya dhamira ya kampuni hiyo katika kusogeza huduma za bima ya maisha karibu zaidi na wananchi, hususan katika kuongeza upatikanaji na uelewa wa huduma hizo nchini.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Alliance Life Assurance Ltd, Byford Mutimusakwa, amesema kufunguliwa kwa ofisi hiyo mpya ni sehemu ya mkakati mpana wa kampuni ya kupanua huduma zake nchini, pamoja na kuleta suluhisho bunifu za bima ya maisha zinazolenga kuwasaidia Watanzania kujenga usalama wa kifedha kwa sasa na baadaye.

Mutimusakwa alibainisha kuwa uwepo wa ofisi hiyo Dodoma utarahisisha upatikanaji wa huduma kwa wateja wa Mkoa wa Dodoma na mikoa jirani, sambamba na kuboresha utoaji wa huduma za ushauri wa kifedha na bima.

Ofisi hiyo mpya iko katika Ghorofa ya Kwanza ya Jengo la Kisangani, Barabara ya Majengo, jijini Dodoma, na inatarajiwa kuwa kitovu muhimu cha huduma za bima ya maisha kwa wananchi wa eneo hilo na maeneo ya jirani.

Aidha, kampuni hiyo imewahimiza wananchi kujitokeza katika ofisi hiyo mpya kupata elimu na ushauri wa kitaalamu kuhusu huduma mbalimbali za bima ya maisha zinazolenga kulinda mustakabali wa kifedha wa familia na jamii kwa ujumla.












Top News