WAZIRI wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar, ameagiza wadau wote katika masoko ya mitaji na dhamana wazingatie sheria na kanuni za masoko ya fedha huku wakiimarisha utoaji wa huduma kwa njia ya kidigitali.

Akizungumza Jumanne wakati wa sherehe ya 5 ya kuhitimisha kozi ya Cheti cha Sekta ya Dhamana na Shindano la Vyuo Vikuu na Taasisi za Elimu ya Juu, Balozi Omar alisisitiza haja ya kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu masoko ya mitaji na dhamana ili kuongeza uelewa na ushiriki.

“Nawaasa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) na wadau kuendelea kutoa elimu kwa umma ili kuongeza uelewa na ushiriki katika sekta hii,” alisema. 

Pia aliagiza CMSA kutekeleza kikamilifu majukumu yake ya kusimamia, kuratibu na kuendeleza masoko ya mitaji na dhamana ili kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa 2050.

Balozi Omar alibainisha kwamba uelewa zaidi wa masoko ya mitaji ni muhimu ili kuhamasisha ushiriki wa Watanzania, akieleza kuwa masoko haya yana nafasi muhimu katika upatikanaji wa mitaji kwa makampuni ya umma na binafsi. Hii inawawezesha wananchi kushiriki moja kwa moja katika uchumi na kuchangia kufanikisha malengo ya Dira ya 2050.

Aliongeza kuwa, kama ilivyo kwa sekta nyingine, masoko ya mitaji na dhamana yanahitaji wataalamu wenye ujuzi na weledi wa kutosha ili kuwezesha upatikanaji wa mitaji ya muda mrefu kwa maendeleo ya uchumi wa kisasa. Alisema kuwa hadi Desemba mwaka jana, jumla ya thamani ya uwekezaji katika masoko ya mitaji ilifikia shilingi trilioni 63.15.

Awali, Mwenyekiti wa Bodi ya CMSA, Lucas Mwimo, alishukuru serikali kwa kuweka mazingira bora yanayowezesha mamlaka kukuza sekta ya masoko ya mitaji. Bw Mwimo alibainisha jitihada za CMSA kutoa mafunzo, kuanzisha bidhaa bunifu, na kuhamasisha ushiriki wa soko wa ndani na nje ya nchi.

Mkurugenzi Mtendaji wa CMSA, CPA. Nicodemus Mkama, alibainisha kuwa wahitimu wa kozi hiyo wanakidhi viwango vya kimataifa, na hivyo kuimarisha ujuzi wa wataalamu wanaotoa huduma katika masoko ya mitaji. “Kuhakikisha tunatoa elimu bora na kujenga uwezo wa wataalamu kunalingana na utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050, inayolenga kuendeleza wataalamu wenye weledi,” alisema.

CMSA pia ilianzisha Shindano la Vyuo Vikuu la Masoko ya Mitaji, lililoshirikisha wanafunzi kote nchini kupitia maswali ya mtandaoni. Jumla ya wanafunzi 28,383 walishiriki, ikizidi malengo kwa zaidi ya asilimia 140. Washindi watano wa juu walipatiwa zawadi za fedha kuanzia shilingi milioni 3 hadi 700,000, na pia watapata mafunzo nchini Nigeria pamoja na kutembelea makampuni makubwa yanayojihusisha na masoko ya mitaji.

Ili kuongeza idadi ya wataalamu waliokidhi viwango vya kimataifa, CMSA inashirikiana na Chartered Institute for Securities & Investment (CISI).

Akizungumza, Naibu Gavana  wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Yamungu Kayandabila, alisisitiza umuhimu wa ujumuishaji wa kifedha na elimu ya kifedha. “Mitandao ya kidigitali imebadilisha mfumo wa kifedha, ikiruhusu elimu ya kifedha mtandaoni. Kufunga pengo la kifedha kidijitali kati ya vijijini na mijini ni jambo kuu katika sera yetu ya fedha na mfumo wa kitaifa wa ubunifu wa kifedha,” alisema.




Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo imepitisha randama ya mpango na makadirio ya bajeti ya matumizi ya kawaida pamoja na mpango wa maendeleo kwa mwaka wa fedha 2026/2027 wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. 

Mpango huo umepitishwa na kamati Machi 24, 2026 chini ya Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Husna Sekiboko,  ambae amesema mpango huu unakwenda  kuwa chachu ya kuandaa vijana wenye ujuzi.

Mhe. Sekiboko amesisitiza kuhakikisha mtiririko wa fedha utakaowezesha miradi yote ya maendeleo inatekelezwa na kukamilika kwa wakati. 

" kwakweli tumeshuhudia  miradi mingi mikubwa mizuri ambayo inajenga imani ya wananchi kwa Serikali na kuongeza tija katika maendeleo," amesema Mhe Sekiboko

Pia ameiomba Wizara kushirikiana kwa Karibu na Wizara ya Fedha kuhakikisha fedha za miradi ya maendeleo kwa sekta ya elimu zinatolewa kwa wakati. Na kwa mtiririko unaowezesha utekelezaji wenye ufanisi.

Kwa upande wake, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, amewashukuru wajumbe wa Kamati hiyo kwa kupokea na kupitisha randama ya bajeti ya wizara na kuahidi kuwa wizara itaendelea kuboresha mifumo na mazingira ya utoaji elimu  ili kuhakikisha kila mtoto wa Kitanzania anapata elimu na ujuzi kwa usawa na ujumuishi.















Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imesisitiza kuimarishwa kwa ushirikiano kati ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na Chuo Kikuu cha Vienna  katika nyanja za sayansi na teknolojia, ikiwemo nishati ya jua, ili kuzalisha wataalamu wenye ujuzi kwa manufaa ya pande zote mbili.

Hayo yameelezwa na Naibu Makamu Mkuu wa Chuo (Taaluma) kutoka UDSM, Prof. Rose Upor alipofanya mazungumzo na  Ujumbe wa Austria ulioongozwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje anayeshughulikia masuala ya kisiasa, Mhe. Balozi Dkt. Hannah Liko, ulipotembelea chuoni hapo  Machi 24, 2026 kwa lengo la kuimarisha ushirikiano katika sekta ya elimu kati ya Tanzania na Austria.

Prof. Upor amesema ili kuimarisha zaidi ushirikiano uliopo kati ya UDSM  na Chuo Kikuu cha Vienna, kuna umuhimu wa kuongeza ufadhili wa masomo katika kada mbalimbali pamoja na kubadilishana wataalamu watakaoweza kufundisha hata kwa njia ya mtandao. 

Naye Balozi na Mwakilishi wa Kudumu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mjini Vienna, Balozi Naimi S.H. Aziz, amesema kuwa ushirikiano kati ya Tanzania na Austria katika sekta ya elimu una mchango mkubwa katika kukuza ujuzi, kuimarisha taasisi na kuongeza ubora wa huduma nchini.

Kwa upande wake, Dkt. Liko amepongeza ushirikiano uliopo kati ya UDSM na Chuo Kikuu cha Vienna, huku akipendekeza kuanzishwa kwa mafunzo ya lugha ya Kijerumani katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Amesema kuwa kuimarika kwa ushirikiano katika sekta ya elimu kutachangia maendeleo ya kiuchumi na kidiplomasia kwa mataifa yote mawili.

Ushirikiano kati ya UDSM na Chuo Kikuu cha Vienna unalenga maeneo manne makuu ya kimkakati, yakiwemo ubadilishanaji wa wanafunzi ili kuwapatia uzoefu wa kimataifa, ubadilishanaji wa wafanyakazi wa kitaaluma na kiutawala, utekelezaji wa tafiti za pamoja zinazogusa changamoto za kimataifa kama utawala bora na maendeleo endelevu, pamoja na uchapishaji wa kazi za pamoja za kitaaluma ili kuhakikisha mitazamo ya Afrika inawakilishwa vyema kimataifa.















Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekabidhi msaada wa tani 500 za mahindi kwa Serikali ya Jamhuri ya Msumbiji kufuatia mafuriko yaliyoikumba nchi hiyo kutokana na mvua kubwa zilizonyesha.

Msaada huo umekabidhiwa Machi 24, 2026 na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Mahmoud Thabit Kombo (Mb) kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Shehena hiyo ya mahindi iliwasili jijini Maputo na ndege ya mizigo ya Shirika la Ndege la Tanzania na kupokelewa na Ujumbe wa Serikali ya Msumbiji uliongozwa na Waziri wa Mipango na Maendeleo, Mhe. Salim Cripton Valá,

Akikabidhi msaada huo, Mhe. Kombo alielezea uhusiano wa karibu na wakindugu uliopo baina ya Tanzania na Msumbiji ulioasisiwa tokea enzi za waasisi wa mataifa hayo mawili, Baba wa Taifa, Hayati Mwl. Juliaus Kambarage Nyerere na Hayati Edward Mondlane. Waziri Kombo alisema kufuatia udugu huo, Rais Dkt. Samia amemtuma kufikisha msaada huo ili uweze kuwapunguzia adha waathirika wa mafuriko hayo.

"Kwa niaba ya Serikali ya Tanzania, Rais Samia anatoa salamu za pole kwa Rais wa Msumbiji, Mhe. Daniel Chapo na watu wa Msumbiji kwa ujumla kutokana na madhila yaliyosababishwa na mafuriko haya na ameahidi kuwa Tanzania ipo tayari kundelea kutoa msaada kwa Msumbiji katika nyakati zote", Waziri Kombo alisema.

Wakati wa ziara hiyo, Mhe. Kombo alipata nafasi ya kukutana na kuzungumza na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Msumbiji Mhe. Maria Belvinda Levy kuhusu kuendeleza na kuimarisha uhusiano na ushirikiano baina ya nchi hizi mbili, hususani kwenye masuala ya kiuchumi.

Serikali ya Msumbiji imetoa shukrani za dhati kwa kupokea msaada huo kutoka kwa ndugu zao Watanzania ambao unabainisha taswira ya ukaribu na ushirikiano wa kweli uliopo baina ya nchi mbili hizi.





















 


Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC), Masanja Kadogosa, leo Machi 24, 2026 ameongoza ziara ya ukaguzi wa mradi wa Canadian Village Awamu ya Kwanza uliopo wilayani Kinondoni, jijini Dar es Salaam.


Mradi huo unaotekelezwa katika eneo lenye ukubwa wa takribani ekari 6.4, ni miongoni mwa miradi inayolenga kukuza uwekezaji wa mitaji ya umma na kuboresha miundombinu ya makazi ya kisasa.


Akizungumza wakati wa ukaguzi huo, Kadogosa alisisitiza umuhimu wa kuhakikisha miradi ya aina hiyo inatekelezwa kwa kuzingatia thamani ya fedha, ubora wa kazi, pamoja na kukamilika kwa wakati ili kuwanufaisha wananchi kama ilivyokusudiwa. Alieleza kuwa kamati itaendelea kusimamia kwa karibu utekelezaji wa miradi yote ya uwekezaji wa umma nchini.


Kwa upande wake, Naibu anayehusika na masuala ya ujenzi, Mhe. Msonde, alieleza kuwa maendeleo ya mradi huo yanaendelea vizuri, huku akibainisha kuwa jitihada zinafanyika kuhakikisha changamoto zinazojitokeza zinatatuliwa kwa wakati ili kuepusha ucheleweshaji.


Aidha, aliongeza kuwa kukamilika kwa mradi huo kutachangia kwa kiasi kikubwa katika kuboresha mazingira ya makazi pamoja na kuongeza thamani ya uwekezaji katika eneo hilo.


Ziara hiyo ni sehemu ya jukumu la Kamati ya PIC kuhakikisha kuwa uwekezaji wa mitaji ya umma unaleta tija, unazingatia uwajibikaji, na unachochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.






Top News