Rais wa Jamhuri ya Namibia, Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah, amewasili nchini kwa Ziara ya Kitaifa ya siku tatu kuanzia tarehe 19 hadi 21 Juni 2026, kwa mwaliko wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), jijini Dar es Salaam, Mhe. Dkt. Nandi-Ndaitwah alipokelewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo, pamoja na viongozi wengine waandamizi wa Serikali. Katika mapokezi hayo pia alikuwepo Balozi wa Jamhuri ya Namibia nchini Tanzania, Mhe. Gabriel Sinimbo.

Ziara hiyo inafanyika katika kipindi ambacho Tanzania na Namibia zinaendelea kuimarisha uhusiano wao wa kihistoria uliojengwa katika misingi ya mshikamano wa harakati za ukombozi wa Afrika, urafiki wa muda mrefu na ushirikiano wa karibu katika nyanja mbalimbali za maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Akiwa nchini, Mhe. Rais Nandi-Ndaitwah anatarajiwa kufanya mazungumzo ya uwili na mwenyeji wake, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa lengo la kuimarisha zaidi ushirikiano katika sekta mbalimbali zenye manufaa kwa wananchi wa Tanzania na Namibia. Viongozi hao pia wanatarajiwa kushuhudia utiaji saini wa hati mbalimbali za makubaliano ya ushirikiano kati ya nchi hizo mbili.

Ziara hii ya kwanza ya Kitaifa ya Rais Nandi-Ndaitwah nchini Tanzania tangu alipoingia madarakani inaashiria dhamira ya pamoja ya Tanzania na Namibia ya kuendeleza ushirikiano wa kimkakati, kuimarisha diplomasia ya uchumi, pamoja na kukuza biashara na uwekezaji kwa manufaa ya pande zote mbili.

Ziara hii pia inatarajiwa kutoa fursa ya kuenzi historia ya ushirikiano wa ukombozi kati ya Tanzania na Namibia, huku ikifungua ukurasa mpya wa ushirikiano katika nyanja mbalimbali za maendeleo kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho cha wananchi wa mataifa hayo mawili.



Na Karama Kenyunko, Michuzi TV

Mkurugenzi wa Uendeshaji wa MSI Tanzania, Dkt. Stephen Mutegeki, amesema utekelezaji wa Programu ya Scaling Up Family Planning (SuFP) umeonyesha kuwa maendeleo makubwa yanawezekana pale wadau mbalimbali wanaposhirikiana katika kufikia malengo ya pamoja.

Akizungumza katika kongamano la kujifunza na kutathmini mafanikio ya programu hiyo lililofanyika jijini Dodoma, Dkt. Mutegeki alisema MSI Tanzania itaendelea kushirikiana na serikali na wadau wengine kuhakikisha mafanikio yaliyopatikana yanaendelezwa na kwamba huduma bora na zenye usawa za afya ya uzazi zinaendelea kuwafikia wananchi wote.

Kwa upande wake, Naibu Mkurugenzi wa Maendeleo wa Ubalozi wa Uingereza nchini Tanzania, Will Guest, alisema Serikali ya Uingereza itaendelea kuunga mkono juhudi za kuboresha afya ya uzazi na haki za wanawake na wasichana.

Alisema kupitia SuFP, zaidi ya wanawake na wasichana milioni 5.2 walifikia huduma za uzazi wa mpango, hatua iliyosaidia kuzuia zaidi ya vifo vya wajawazito 6,500 na mimba zisizotarajiwa milioni 8.3.

Akizungumza kwa niaba ya washirika wa utekelezaji, Mwakilishi Mkazi wa UNFPA nchini, Mark Bryan Schreiner, alisema mafanikio ya programu hiyo yamethibitisha kuwa maendeleo makubwa yanawezekana pale serikali, watoa huduma, washirika wa maendeleo na jamii wanaposhirikiana.

Kwa mujibu wa washirika hao, mafanikio yaliyopatikana kupitia SuFP yametokana na ushirikiano wa karibu kati ya Serikali na wadau mbalimbali, wakiwemo MSI Tanzania, UNFPA, Serikali ya Uingereza kupitia FCDO, EngenderHealth na Pathfinder International.

Programu ya SuFP iliyotekelezwa kuanzia mwaka 2017 hadi 2026 kwa ufadhili wa Serikali ya Uingereza kupitia FCDO, ilitekelezwa kwa ushirikiano wa Serikali ya Tanzania na taasisi za EngenderHealth, UNFPA, MSI Tanzania na Pathfinder International.

Mkurugenzi uendeshaji wa MSI Dkt. Stephen Mutegeki





Na Karama Kenyunko, Michuzi TV

SERIKALI imeahidi kuendelea kuimarisha na kutekeleza huduma za uzazi wa mpango pamoja na afya ya uzazi, mama, mtoto na vijana ili kuhakikisha mafanikio yaliyopatikana kupitia Mradi wa Scaling Up Family Planning (SuFP) yanaendelea kudumu hata baada ya mradi huo kufikia tamati.

Kauli hiyo imetolewa mkoani Dodoma na Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Grace Magembe, kwa niaba ya Waziri wa Afya, wakati wa kongamano la kujifunza na kutathmini mafanikio ya Mradi wa SuFP lililofanyika jijini Dodoma baada ya utekelezaji wa miaka tisa.

Dkt. Magembe amesema serikali imejipanga kuhakikisha huduma hizo zinaendelea kutolewa kwa ubora katika ngazi zote za utoaji huduma kwa kuwa wananchi wanaendelea kuzihitaji bila kujali kama mradi umefungwa au la.

“Tunapozungumzia kufungwa kwa mradi, haimaanishi kufungwa kwa huduma. Watu wanaohitaji huduma bado wapo, hivyo jukumu letu kama serikali na wadau ni kuhakikisha huduma zinaendelea kutolewa kwa ufanisi na ubora uleule,” amesema.

Ameeleza kuwa serikali tayari imeonyesha dhamira yake kwa kuongeza mchango katika ununuzi wa bidhaa za uzazi wa mpango sambamba na kuzijumuisha katika mipango na bajeti za afya ili kuhakikisha upatikanaji wake unaendelea bila kukwama.

Katika hatua nyingine, Dkt. Magembe amewataka Waganga Wakuu wa Mikoa (RMOs), Waganga Wakuu wa Wilaya (DMOs) na Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhakikisha huduma za afya ya uzazi na uzazi wa mpango zinaendelea kupewa kipaumbele katika mipango na bajeti za maendeleo.

Ameonya kuwa kutoweka kipaumbele kwa huduma hizo kunaweza kusababisha kuongezeka kwa mimba za utotoni, vifo vya uzazi, kuacha shule kwa wanafunzi na changamoto nyingine za afya ya uzazi.

“Wananchi hawajui kama mradi umeisha au kuna changamoto za fedha. Wanachojua ni kwenda katika kituo cha afya na kupata huduma bora. Hilo ndilo jukumu letu sote kuhakikisha linatimia,” amesema.

Pia amepongeza juhudi za Rais Samia Suluhu Hassan, ambaye ni Bingwa wa Umoja wa Afrika katika Afya ya Mama, Mtoto na Mchanga, akisema mafanikio yaliyopatikana nchini yanapaswa kutumika kama mfano kwa mataifa mengine barani Afrika.






WAZIRI Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka wafugaji nchini kuanzisha mashamba ya malisho na kutumia teknolojia za kisasa za ufugaji ili kuongeza tija na kupata suluhisho la kudumu la migogoro kati ya wakulima na wafugaji inayochangiwa na ongezeko la matumizi ya ardhi.

Akifungua Maonesho ya Tri-Nations Livestock Expo yaliyofanyika Ubena Zomozi, Wilaya ya Chalinze mkoani Pwani, Ijumaa Juni 19, 2026, Dkt. Mwigulu amesema ongezeko la idadi ya watu na matumizi ya ardhi linaifanya nchi kutafuta mbinu endelevu za kuhakikisha shughuli za ufugaji zinaendelea kwa tija bila kuibua migogoro.

"Hata tusingependa kufanya hivyo, hatuna njia nyingine kwa sababu ongezeko la matumizi ya ardhi linalosababishwa na ongezeko la idadi ya watu, huku ardhi ikiwa haiongezeki, linatulazimu kutafuta suluhisho endelevu," amesema Dkt. Mwigulu.

Amesema changamoto ya upatikanaji wa malisho inapaswa kwenda sambamba na matumizi ya mbegu bora za mifugo na malisho ili kuwawezesha wafugaji kupata maziwa mengi na nyama nyingi hata kwa kuwa na mifugo michache.

Aidha, Dkt. Mwigulu amewataka wafugaji wa Kitanzania kuyatumia maonesho hayo kama shamba darasa la kujifunza ufugaji bora, wa kisasa na wenye tija ili kuongeza uzalishaji na mchango wa sekta hiyo katika uchumi wa Taifa.

Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu ametoa wito kwa wadau wa sekta ya mifugo nchini kuchangamkia fursa za matumizi ya teknolojia za kisasa za ufugaji ili kuongeza uzalishaji na kukuza uchumi.

"Maonesho hayo yanapaswa kutumika kama darasa la teknolojia na jukwaa muhimu la kununua na kuuza mifugo bora kupitia minada inayoambatana na matukio hayo," amesema.

Pia, amewataka wazalishaji kuacha utamaduni wa kuandaa bidhaa zenye ubora wa hali ya juu kwa ajili ya maonesho pekee na badala yake waufanye ubora huo kuwa utaratibu wa maisha yao ya kila siku ya kibiashara.

"Ninachokisema ni nini? Tulichokiona katika maonesho haya ndio uwe utaratibu wa maisha. Tusiwe na bidhaa tu kwa ajili ya maonesho; bidhaa za aina hii ndio ziwe bidhaa za kila siku katika maisha yetu," amesisitiza Dkt. Mwigulu.

Kwa upande mwingine, Dkt. Mwigulu amepongeza mchango wa sekta binafsi katika kuleta maendeleo na mageuzi ya kiuchumi katika sekta ya mifugo, akitaja Mbogo Ranch kuwa mfano wa kuigwa.

Vilevile, amesema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameondoa zaidi ya kodi 300 zilizokuwa zikigusa sekta mbalimbali za uzalishaji kwa lengo la kuendeleza sekta hizo, ikiwemo sekta ya mifugo na sekta nyingine zinazohusiana na uzalishaji.

Kwa Upande wake Waziri wa Mifugo Dkt. Bashiri Kakurwa amempongeza Rais Dkt.Samia Suluhu Haasan kwa jitihada zake za kuhakikisha anaikuza na kuiendeleza sekta ya mifugo nchini 

Aidha, Amsemea kuwa lengo kuu la maonesho hayo ni kujenga mfungo imara wa biashara wa mifugo na mazao yake kwa kuwakutanisha wafugaji na wafanyabiashara na wadau wote katika mnyororo wa thamani wa sekta ya mifugo ili kubadlishana uzoefu na kujifunza mbinu za kisasa za ufugaji pamoja na kupanua fursa za masoko nchini

Naye Waziri Mkuu Mstaafu Frederick Sumaye, amesema sekta ya mifugo ni muhimu sana katika uchumi wa nchi na inahitaji kusimamiwa vizuri ili iweze kutoa mchango mkubwa zaidi katika maendeleo ya Taifa.













 

Na Mwandishi Wetu

Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) imesema matumizi ya Mfumo wa Stakabadhi za Ghala katika sekta ya mifugo yataimarisha masoko na kuongeza ushindani wa bei ya bidhaa hiyo nchini.

Akizungumza Juni 19, 2026 katika Maonesho ya Mifugo na Mnada wa Kimataifa yanayofanyika katika Shamba la Mbogo, Chalinze mkoani Pwani, Afisa Ubora wa WRRB, Anatolius Kabyemera, amesema bodi hiyo imeingia kwenye sekta hiyo kwa lengo la kuwawezesha wafugaji kuuza mifugo yao kupitia mfumo rasmi na wenye tija.

Amesema mfumo huo utasaidia wafugaji kuimarisha ufugaji na kuongeza kipato chao ambapo mifugo itahifadhiwa kwenye eneo maalumu lililosajiliwa kama ghala ya mifugo wakati wakisubiri mnada.

“Mfumo huu utawezesha mifugo kuletwa kwenye ghala ambalo ni eneo teule lenye maji, malisho na wataalamu wa mifugo, litahesabika kuwa ghala la mifugo. Baada ya mfugaji kuingiza mifugo yake katika ghala akisubiri mnada, atapatiwa stakabadhi itakayomwezesha kupata mkopo kupitia taasisi za fedha ambazo tumeshaingia nazo makubaliano, kwa mfano NBC,” amesema Kabyemera.

Kwa upande wake, mmoja wa wafugaji waliotembelea banda la WRRB katika maonesho hayo, Moringe Gasper, ameipongeza bodi hiyo kwa kutoa elimu kuhusu matumizi ya mfumo huo katika sekta ya mifugo.

Amesema wafugaji wengi wako tayari kuona utekelezaji wa mfumo huo unaanza haraka ili nao waweze kunufaika kama ilivyo kwa wakulima wanaotumia mfumo wa stakabadhi za ghala kwa sasa.






Na Mwandishi Wetu

Mchezaji wa Kimataifa wa Timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars), Simon Msuva, amepongeza mpango wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) wa kuandaa mafunzo maalum kwa Waandishi wa Habari kuelekea Mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027), akisema hatua hiyo itasaidia kuimarisha mchango wa sekta ya habari katika kuitangaza Tanzania, kukuza vipaji vya wanamichezo na kuibua fursa mbalimbali za maendeleo zitakazotokana na mashindano hayo.

Msuva ametoa pongezi hizo leo, tarehe 19 Juni 2026, alipotembelea Ofisi za Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari zilizopo Posta Mpya, Mtaa wa Jamhuri jijini Dar es Salaam na kufanya mazungumzo na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi hiyo, Wakili Patrick Kipangula.

Amesema Waandishi wa Habari wamekuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya michezo nchini kwa kutangaza vipaji vya wanamichezo, kuhamasisha ushiriki wa wananchi katika michezo na kuitangaza Tanzania ndani na nje ya nchi.

“Mimi nawaombea waweze kutengeneza elimu ya kutosha kwa Waandishi wa Habari kwa sababu hawa Waandishi wa Habari wametufanya sisi tuinuke. Bila wao leo hii huenda nisingefahamika kama Simon Msuva. Wana nafasi kubwa sana katika nchi yetu, lakini pia wanahitaji kuendelea kupata elimu na mafunzo yatakayowasaidia kuwa bora zaidi katika kazi yao,” amesema Msuva.

Msuva amesema AFCON 2027 ni zaidi ya mashindano ya mpira wa miguu kwani yatatoa fursa katika sekta mbalimbali ikiwemo biashara, utalii, uwekezaji na ajira, hivyo kuna umuhimu wa Waandishi wa Habari kuandaliwa mapema ili waweze kuripoti kwa weledi na kusaidia wananchi kuelewa na kutumia fursa zitakazojitokeza.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, amemshukuru Msuva kwa kutembelea Bodi hiyo na kuunga mkono juhudi za kuimarisha taaluma ya habari kuelekea AFCON 2027.

Amesema JAB imeanza maandalizi ya mafunzo maalum kwa Waandishi wa Habari za michezo na kada nyingine za habari kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kuripoti mashindano hayo kwa viwango vya kimataifa pamoja na kuibua na kuhabarisha umma kuhusu fursa za maendeleo zitakazotokana na AFCON 2027.

Wakili Kipangula amesema kupitia mafunzo hayo, Waandishi wa Habari watawezeshwa kuelewa kwa kina mchango wa michezo katika maendeleo ya taifa, uchumi wa michezo, utalii, uwekezaji na maeneo mengine muhimu yatakayochochewa na mashindano hayo makubwa ya bara la Afrika.

Tanzania kwa kushirikiana na Kenya na Uganda inatarajiwa kuwa mwenyeji wa Mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) mwaka 2027, hatua inayofungua fursa kubwa za kiuchumi na kijamii kwa wananchi na taifa kwa ujumla.





Na Janeth Raphael MichuziTv

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameitaka Mahakama ya Tanzania kuendelea kuimarisha misingi ya haki, nidhamu, uwajibikaji na maadili katika utoaji wa huduma za haki ili kuhakikisha mfumo imara na wa kuaminika wa utoaji haki nchini.

Rais Samia ametoa wito huo leo Ikulu jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya kumuapisha Dkt. John Anthony Jingu kuwa Mtendaji Mkuu mpya wa Mahakama ya Tanzania.

Amesema Serikali itaendelea kuiwezesha Mhimili wa Mahakama kupitia maboresho ya mifumo, uboreshaji wa miundombinu pamoja na rasilimali watu, akibainisha kuwa hatua hizo zimekuwa na mchango mkubwa katika kuongeza ufanisi na kuboresha huduma za utoaji haki nchini.

Katika hotuba yake, Rais Samia pia amemtaka Dkt. Jingu kuendeleza mafanikio yaliyofikiwa na mtangulizi wake, Profesa Elisante Ole Gabriel, ambaye amestaafu baada ya kulitumikia taifa katika nafasi hiyo.

Amemshukuru Profesa Gabriel kwa mchango wake mkubwa katika kuimarisha mifumo ya kiutendaji ndani ya Mahakama, akisema ameacha msingi imara unaopaswa kuendelezwa kwa maslahi ya wananchi na mfumo wa haki kwa ujumla.

Aidha, Rais Samia amempongeza Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju, kwa uongozi wake unaoendelea kusimamia Mahakama kwa ufanisi, weledi na maadili, hatua inayosaidia kuimarisha heshima na hadhi ya mhimili huo wa haki nchini.

Vilevile, amewasisitiza viongozi wote wa Mahakama nchini kuendeleza nidhamu na uwajibikaji ili kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa wakati, kwa heshima na kwa kuzingatia matakwa ya sheria.



 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na viongozi mbalimbali kwenye picha na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Dkt. John Anthony Jingu, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 19 Juni, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na kwenye picha na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Dkt. John Anthony Jingu pamoja na Mtendaji Mkuu Mstaafu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elistante Ole Gabriel mara baada ya hafla ya Uapisho,  Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 19 Juni, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akizungumza na viongozi mbalimbali baada ya kumuapisha Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Dkt. John Anthony Jingu, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 19 Juni, 2026.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Dkt. John Anthony Jingu akiapa Kiapo cha Maadili pamoja na Karani wa Baraza la Mawaziri Bw. Francis Petro Mossongo,  Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 19 Juni, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akimuapisha Dkt. John Anthony Jingu kuwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 19 Juni, 2026.





Na Janeth Raphael MichuziTv 

Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA), kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha pamoja na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), imeboresha utoaji wa huduma zake kwa kuanzisha moduli maalumu ndani ya Mfumo wa Kitaifa wa Ununuzi wa Kielektroniki (NeST) inayowawezesha wananchi kuwasilisha malalamiko na rufaa za zabuni popote walipo nchini.

Akizungumza leo jijini Dodoma wakati wa katika maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma katika banda la PPAA, Katibu Mtendaji wa PPAA, James Sando, alisema hatua hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa mkakati wa serikali wa kutumia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kuboresha upatikanaji wa huduma kwa wananchi.

Amesema PPAA imeamua kuendana na kasi ya maendeleo ya teknolojia kwa kuwa haiwezi kujitenga na mageuzi ya kidijitali yanayoendelea nchini, huku serikali ikiweka msisitizo mkubwa katika kuhakikisha huduma za umma zinapatikana kwa urahisi, haraka na kwa ufanisi zaidi.

“Tunachokifanya ni kutekeleza maelekezo tuliyoyapokea kutoka serikalini na kuhakikisha wananchi wanapata huduma zenye ufanisi mkubwa. Mfumo huu pia utatusaidia kutatua changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika usimamizi wa rufaa na malalamiko ya zabuni,” amesema Sando.

Amefafanua kuwa moduli hiyo ilianza kutumika rasmi mwezi Februari mwaka 2025 baada ya kuzinduliwa na Waziri wa Fedha wa wakati huo, ambaye amesisitiza matumizi ya TEHAMA katika utoaji wa huduma za umma ili kuongeza uwazi, uwajibikaji na urahisi wa upatikanaji wa huduma kwa wananchi.

Kwa mujibu wa Sando, matumizi ya mfumo huo yamepunguza utegemezi wa taratibu za ana kwa ana, hivyo kuwapa wananchi na wadau wa sekta ya ununuzi wa umma fursa ya kuwasilisha malalamiko na rufaa zao kwa njia ya mtandao bila kulazimika kusafiri hadi katika ofisi za PPAA.

Amesema PPAA itaendelea kuboresha huduma zake za kidijitali ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora zaidi, huku taasisi hiyo ikipata uwezo mkubwa wa kushughulikia na kutatua migogoro ya zabuni kwa wakati na kwa ufanisi.

“Lengo letu ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora, za haraka na zenye uwazi, sambamba na kuimarisha utatuzi wa changamoto zinazohusiana na rufaa na malalamiko ya zabuni za umma,” amesisitiza Sando.



Bahi, Dodoma. Serikali imeipongeza NMB Bank Plc kwa kujenga shule ya sekondari ya bweni kwa wanafunzi wenye mahitaji maalumu wilayani Bahi, mradi wa Sh5 bilioni uliokamilika kwa asilimia 100.

Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Elimu, Atupele Mwambene, amesema shule hiyo imejengwa kwa kiwango cha juu na ina mabweni, vitanda, madawati pamoja na uwezo wa kuhudumia wanafunzi 160. Inatarajiwa kuanza kupokea wanafunzi Januari 2027 baada ya usajili.

Mkurugenzi wa Uhusiano na Wawekezaji, Uendelevu na Mawasiliano wa NMB, Innocent Yonazi, amesema mradi huo unalenga kupanua fursa za elimu kwa watoto wenye mahitaji maalumu. NMB imetoa zaidi ya Sh24 bilioni kwa miradi ya kijamii katika miaka mitano.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Bahi, Albina Mtumbuka, amesema halmashauri iko tayari kuipokea na kuitunza shule hiyo, huku akiwataka wazazi kutowaficha watoto wenye mahitaji maalumu.












Top News