Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi akizungumza leo Machi 27, 2026 jijini Dar es Salaam katika Mkutano wa Uhakiki wa Rasimu ya Mpango wa Pili wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji (MKUMBI II).
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo, akizungumza leo Machi 27, 2026 jijini Dar es Salaam katika Mkutano wa Uhakiki wa Rasimu ya Mpango wa Pili wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji (MKUMBI II).


Na Mwandishi Wetu
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, amesema Mpango wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji (MKUMBI) umeendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuimarisha mazingira ya uwekezaji na biashara nchini, hatua inayochochea ukuaji wa uchumi na kuvutia wawekezaji wa ndani na nje.

Dk. Mwinyi ameyasema hayo Machi 27, 2026 jijini Dar es Salaam wakati akizungumza katika Mkutano wa Uhakiki wa Rasimu ya Mpango wa Pili wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji (MKUMBI II), ambapo alieleza kuwa mpango huo umewezesha sekta mbalimbali kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi katika kuweka mazingira rafiki ya biashara.

Amesema kupitia maboresho hayo, Serikali imeendelea kuweka misingi imara ya kuvutia uwekezaji huku ikilenga kufikia malengo ya Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 inayokusudia kuifikisha Tanzania kwenye uchumi wa kipato cha juu.

Kwa mujibu wa Dk. Mwinyi, dira hiyo inalenga kufikia uchumi wenye thamani ya dola za Marekani trilioni moja pamoja na kipato cha wastani wa dola 7,000 kwa kila Mtanzania ifikapo mwaka 2050.

Amesisitiza kuwa ili kufikia malengo hayo, nchi inalazimika kuhakikisha ukuaji wa Pato la Taifa unafikia angalau asilimia 10 kwa mwaka kuanzia 2026 hadi 2050, jambo litakalowezekana kupitia uwekezaji mkubwa katika sekta za uzalishaji, viwanda, kilimo cha kisasa, uchumi wa buluu, nishati na TEHAMA.

“Ni wazi kuwa Serikali pekee haiwezi kufanikisha malengo haya, hivyo ushiriki wa sekta binafsi ni muhimu sana katika kuongeza uzalishaji, ajira na mapato ya taifa,” alisema.

Aidha, amebainisha kuwa takwimu zinaonesha mafanikio ya maboresho ya mazingira ya biashara, akitolea mfano mwaka 2024 ambapo miradi 901 ya uwekezaji yenye thamani ya dola bilioni 9.3 ilisajiliwa na kuzalisha ajira zaidi ya 212,000.

Ameongeza kuwa katika kipindi cha miaka miwili ya 2024 hadi 2025, miradi 1,828 yenye thamani ya dola bilioni 20.3 ilisajiliwa nchini, hatua inayodhihirisha kuimarika kwa mazingira ya uwekezaji.

Dk. Mwinyi amesema Serikali pia imeendelea kuwekeza katika miundombinu ya kimkakati ikiwemo reli ya kisasa, bandari, barabara, nishati na TEHAMA ili kupunguza gharama za uzalishaji na kuongeza ushindani wa uchumi.


Amesema kupitia MKUMBI, Serikali imefanya mapitio ya sheria zaidi ya 94 na kuondoa au kupunguza zaidi ya tozo na ada 628 zilizokuwa kikwazo kwa wafanyabiashara, hatua iliyosaidia kupunguza urasimu na kuongeza uwazi katika utoaji wa huduma.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo, amesema mafanikio ya kuboresha mazingira ya biashara yatategemea pia mabadiliko ya mitazamo kwa watendaji wa serikali wanaosimamia utekelezaji wa sera na sheria.

Amesema rasimu ya MKUMBI II imebainisha changamoto 59 zinazokwamisha biashara Tanzania Bara na Zanzibar na kupendekeza maeneo 11 ya mageuzi yenye hatua 246 za utekelezaji ili kuboresha zaidi mazingira ya biashara.

Naye Waziri wa Kazi na Uwekezaji Zanzibar, Shariff Ali Shariff, amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeanza kufanya mapitio ya Sheria ya Uwekezaji ya mwaka 2003 pamoja na kuanzisha mifumo ya kidijitali ili kurahisisha huduma kwa wawekezaji wa ndani na nje.

Aidha, baadhi ya wafanyabiashara waliohudhuria mkutano huo walisisitiza umuhimu wa kuondoa vikwazo vinavyokwamisha biashara katika ngazi za halmashauri pamoja na kuhakikisha sekta binafsi inashirikishwa kikamilifu katika utekelezaji wa mpango huo.

Mkutano huo ulilenga kukusanya maoni ya wadau mbalimbali kabla ya kupitishwa kwa rasimu ya mwisho ya MKUMBI II, ambayo inatarajiwa kuwa chombo muhimu katika kuimarisha mazingira ya uwekezaji na kukuza uchumi wa Tanzania.



Matukio mbalimbali katika picha.




Picha za Pamaoja.
Naibu Gavana, Dkt. Yamungu Kayandabila, akijadiliana jambo na Profesa Zhiguo He kutoka Chuo Kikuu cha Stanford Marekani, baada ya ziara ya wanafunzi wa chuo hicho katika ofisi za Benki Kuu jijini Dar es Salaam. Kulia ni Mkurugenzi wa Mifumo ya Malipo ya Taifa, Bi. Lucy Shaidi.

*******************

Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) anayeshughulikia Sera za Uchumi na Fedha, Dkt. Yamungu Kayandabila, amesema kuwa mifumo ya malipo ya Taifa ina mchango mkubwa katika kukuza uchumi jumuishi na kuimarisha ujumuishwaji wa kifedha nchini.

Akitoa hotuba ya ukaribisho kwa wanafunzi wa Shahada ya Uzamili ya Biashara (MBA) kutoka Chuo Kikuu cha Stanford, Marekani, waliotembelea BoT jijini Dar es Salaam, Dkt. Kayandabila alieleza kuwa mifumo ya malipo inachangia ukuaji wa uchumi shirikishi kwa kuwezesha malipo ambayo yanachochea ugavi katika uchumi na kuwa uti wa mgongo wa Uthabiti wa Sekta ya Fedha.

Alibainisha kuwa mifumo ya malipo yenye ufanisi, iliyo salama na shirikishi huchochea ufanisi wa sera ya fedha kwa kuwezesha uenezaji mzuri wa mabadiliko ya viwango vya riba vya Benki Kuu na kuimarisha udhibiti wa ukwasi ndani ya uchumi.

Dkt. Kayandabila alisema Benki Kuu imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kisera na kuwekeza katika miundombinu ili kuimarisha na kuboresha mifumo ya malipo, sambamba na kuchochea ubunifu hususan katika huduma za kifedha za kidijitali na ujumuishwaji wa kifedha.

Akifafanua kuhusu historia ya maboresho hayo, alisema kuwa mchakato wa kisasa wa mifumo ya malipo ulianza katikati ya miaka ya 1990 kama sehemu ya mageuzi mapana ya sekta ya fedha yaliyolenga kuongeza ufanisi, usalama na uthabiti wa mfumo wa fedha.

Aliongeza kuwa mageuzi hayo yaliwezesha kuingia kwa benki binafsi za ndani na za kimataifa, ubinafsishaji wa baadhi ya benki za serikali pamoja na kuondolewa kwa baadhi ya vikwazo katika huduma na bidhaa za kifedha.

Kwa mujibu wa Dkt. Kayandabila, mwaka 1996 BoT ilianzisha Mradi wa Maboresho ya Mifumo ya Malipo ya Taifa uliolenga kubadilisha mfumo wa zamani uliotegemea zaidi fedha taslimu na karatasi kuwa mfumo wa kielektroniki unaoendana na viwango vya kimataifa.

Alikumbusha kuwa kabla ya maboresho hayo, matumizi ya fedha taslimu yalitawala, huku hundi zikichukua hadi siku 14 kukamilisha miamala mikoani na siku 7 jijini Dar es Salaam, hali iliyokuwa ikichelewesha shughuli za kiuchumi.

Aidha, alisisitiza kuwa BoT inaendelea kufuatilia maendeleo ya teknolojia za mifumo ya malipo duniani na kushirikiana na wadau wa kikanda na kimataifa ili kunufaika na ubunifu huo, huku ikiendelea kulinda uthabiti wa sekta ya fedha, uadilifu wa mifumo na maslahi ya watumiaji.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Mifumo ya Malipo ya Taifa, Bi. Lucy Shaidi, akielezea hatua muhimu zilizofikiwa katika safari ya kuendeleza mifumo ya malipo hadi kufikia mwaka 2025, alisema kuwa kumekuwapo na ukuaji wa kasi wa malipo ya papo kwa papo, huduma za fedha kupitia simu za mkononi, pamoja na mifumo ya malipo inayoweza kuunganishwa.

Alibainisha kuwa maendeleo hayo yanaendelea kuichochea Tanzania kuelekea katika mfumo wa fedha uliojumuishi zaidi, wenye ufanisi, na unaotegemea kwa kiasi kikubwa teknolojia za kidijitali.

Miongoni na mafanikio makubwa ya Benki Kuu katika mifumo ya malipo ni kuanzishwa kwa Mfumo wa Malipo ya Papo kwa Hapo (Tanzania Instant Payment System – TIPS) unaoruhusu watumiaji wa huduma za fedha kutuma na kupokea fedha papo hapo , bila kujali taasisi ya kifedha wanayotumia.

TIPS umeongeza ufanisi, umepunguza gharama za miamala, na kuimarisha ujumuishwaji wa kifedha kwa kurahisisha miamala ya kifedha kwa watu binafsi na biashara nchini Tanzania.
Naibu Gavana, Dkt. Yamungu Kayandabila, akifafanua jambo kwa wanafunzi wa Shahada ya Uzamili ya Biashara (MBA) kutoka Chuo Kikuu cha Stanford, Marekani, walipotembelea Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam kujifunza kuhusu Mifumo ya Malipo ya Taifa inayosimamiwa na BoT.
Mkurugenzi wa Mifumo ya Malipo ya Taifa, Bi. Lucy Shaidi, akizungumza wakati wa ziara ya wanafunzi wa Shahada ya Uzamili ya Biashara (MBA) kutoka Chuo Kikuu cha Stanford, Marekani, walipotembelea Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam kujifunza kuhusu Mifumo ya Malipo ya Taifa inayosimamiwa na BoT.
Mkurugenzi wa Ustawi na Huduma Jumuishi za Fedha, Bw. Kennedy Komba, akizungumza wakati wa ziara ya wanafunzi wa Shahada ya Uzamili ya Biashara (MBA) kutoka Chuo Kikuu cha Stanford, Marekani, walipotembelea Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam kujifunza kuhusu Mifumo ya Malipo ya Taifa inayosimamiwa na BoT.
Meneja kutoka Kurugenzi ya Mifumo ya Malipo ya Taifa, Dkt. Willian Mng’ong’ose, akizungumza wakati wa ziara ya wanafunzi wa Shahada ya Uzamili ya Biashara (MBA) kutoka Chuo Kikuu cha Stanford, Marekani, walipotembelea Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam kujifunza kuhusu Mifumo ya Malipo ya Taifa inayosimamiwa na BoT.
Afisa Uhusiano wa Umma kutoka Idara ya Mawasiliano BoT, Bi. Graceana Mahega, akieleza jambo kuhusu makumbusho ya Benki Kuu ya Tanzania kwa wanafunzi wa Shahada ya Uzamili ya Biashara (MBA) kutoka Chuo Kikuu cha Stanford, Marekani, walipotembelea Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam tarehe 27 Machi 2026.


Na Mwandishi Wetu

WALIMU 150 wa amali kwenye shule za serikali wanaondoka Jumapili kwenda nchini India kwa mafunzo maalum ya amali ambayo yatawawezesha kuongeza ujuzi kwenye taaluma hiyo.

Walimu hao kutoka mikoa mbalimbali nchini waliagwa rasmi jana kwenye hafla maalum iliyohudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali.

Waliagwa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolph Mkenda na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, TAMISEMI, Profesa Riziki Shemdoe na Mkurugenzi Mkuu wa Global Education Link, (GEL) Abdulmalik Mollel.

Akizungumzawakati wa hafla ya kuwaaga walimu hao, Profesa Mkenda alisema safari hiyo ni maono ya Rais Samia Suluhu Hassan ambaye amekuwa akisisitiza kuboreshwa kwa elimu ya amali.

Profesa Mkenda alisema kwa kuwa wameanza kutoa mafunzo hayo ya amali ikiwemo kwenda kujifunza kwenye mataifa mbalimbali duniani hakutakuwa na kurudi nyuma.

“Mheshimiwa Rais Samia amesisitiza mara kadhaa kuhusu mafunzo ya amali, anataka kuona tunakwenda mbali zaidi namimi nasema kwa kuwa tumeanza basi hatutarudi nyuma, tutakwenda India na mataifa mbalimbali kujifunza wenzetu wamefanyanini kwenye mafunzo ya amali,” alisema

Aidha, aliwataka walimu hao kujifunza kwa bidii wakiwa nchini India ili watakaporudi wawe mfano kwa walimu wengine ambao hawajapata nafasi hiyo.

“Tunataka kuona mabadiliko makubwa, mtakaporudi watu waone kabisa kwamba kuna watu walikuwa nchini India kwa masomo, mhakikishe shule zinavifaa vya kufundishia masomo ya amali katika ngazi zote,” alisema

“Tunatambua maono makubwa ya rais wetu kwenye masomo ya amali kwa hiyo kazi yetu sisi wasaidizi wake ni kuyatafsiri kwa vitendo kwa kufanya kazi kuhakikisha tunatimiza ndoto hizo kwa kutoa elimu bora na siyo bora elimu,” alisema

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, TAMISEMI, Profesa Riziki Shemdoe alisema kuzingatia nidhamu na maadili watakayofundishwa nchini India kwaajili ya kuja kuleta matokeo chanya kwenye maeneo yao.

“Tunataka mkirudi muwe chachu kwa wengine kutaka nao kwenda India kujifunza, mtushauri tufanye nini ili tuweze kutoa matokeo chanya kwenye maono ya rais Samia,” alisema

Aidha, alisema safari ya walimu hao ni matokeo ya mabadiliko ya mitaala ya elimu yaliyoanza muda mrefu na kuja kutekelezwa na Rais wa awamu ya sita, Rais Samia Suluhu Hassan.

“Mageuzi ya elimu utekelezaji wake ni wa muda mrefu,unamilima na mabonde kwa hiyo ingawa kuna changamoto nyingi lakini sisitutapambana mpaka mwisho hakutakuwa na kurudi nyuma hata siku moja,” alisema Waziri Shemdoe







Dar es Salaam

KAMPUNI ya Airtel Tanzania imezindua rasmi mnara wa mawasiliano wenye teknolojia ya 4G na 5G katika mtaa wa Machimbo, Tabata, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kampuni hiyo kuboresha huduma za mawasiliano na kukuza uchumi wa kidijitali kwa wananchi.

Akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi, Afisa Mtendaji wa Kata ya Machimbo, Bi. Lidya Bwathondi, alisema kuwa uwekezaji huo umeleta mabadiliko makubwa kwa wakazi wa eneo hilo ambao awali walikumbana na changamoto za mawasiliano.

“Kabla ya ujio wa mnara huu, wakazi wa Machimbo walikuwa wanapata shida kupata mawasiliano ya uhakika. Leo hii hali imebadilika, mawasiliano yameimarika na wananchi wanaweza pia kufanya biashara zao mtandaoni kwa urahisi zaidi,” alisema Bwathondi.

Kwa upande wake, Meneja Biashara wa Airtel, Bw. Benson Mbwanga, alieleza kuwa uzinduzi wa mnara huo ni sehemu ya mkakati wa Airtel wa kuendelea kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi pamoja na kuunga mkono jitihada za Serikali katika kuimarisha miundombinu ya mawasiliano nchini.

“Uwekezaji huu unaonesha dhamira ya Airtel ya kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma bora za mawasiliano. Tunaendelea kupanua mtandao wetu wa 4G ili kuwezesha wananchi kuwasiliana kwa urahisi, kufanya biashara za kidijitali na kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kisasa,” alisema Mbwanga.

Baadhi ya wakazi wa mtaa wa Machimbo, akiwemo Bi. Mariam Simon, Bi. Bertha Livingston, Bi. Khadija Seif na Bi. Sada Nyambe, walieleza kufurahishwa kwao na uwekezaji huo wakisema utarahisisha shughuli zao za kila siku, hususan biashara za kidijitali, na kuishukuru Airtel kwa kuchagua kuwekeza katika eneo lao.

Uzinduzi wa mnara huu ni sehemu ya uwekezaji mpana wa Airtel ambapo jumla ya minara mipya tisa yenye teknolojia ya 4G imejengwa jijini Dar es Salaam, ikiwa ni jitihada za kuendelea kuboresha huduma za mawasiliano na kusaidia maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.

Airtel Tanzania inaendelea kujikita katika kutoa huduma bora, za uhakika na zenye ubunifu, huku ikiunga mkono juhudi za Serikali za kuhakikisha upatikanaji wa mawasiliano bora kwa Watanzania wote.




Mbunge wa Jimbo la Kilombero, Abubakari Asenga, ametoa pole kwa wananchi wa jimbo hilo waliokumbwa na mafuriko makubwa yaliyosababishwa na mvua zinazoendelea kunyesha katika maeneo mbalimbali ya Halmashauri ya Mji wa Ifakara, mkoani Morogoro.

Akizungumza leo Machi 27, 2026 katika Ofisi ya Waziri Mkuu inayoshughulikia maafa, Mara baada ya kupokea msaada wa magodoro, mablanketi na chakula, Asenga amesema kuwa juhudi zinaendelea kuhakikisha wananchi waliopata madhara wanapata msaada wa haraka ili kupunguza athari walizokumbana nazo.

Mbunge huyo ameeleza shukrani zake kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, pamoja na Waziri Mkuu, Mwigulu Nchemba, kwa kuwezesha upatikanaji wa vifaa vya dharura kwa ajili ya kuwasaidia waathirika.

Amesema kuwa tayari wamepokea msaada unaojumuisha magodoro 75, mablanketi pamoja na tani 10 za mahindi, ambavyo vitasambazwa kwa wananchi waliokumbwa na mafuriko hayo wakati wakisubiri hatua zaidi za msaada kutoka serikalini.

Aidha, Asenga amewapongeza wananchi pamoja na kamati ya maafa ya wilaya kwa kushirikiana na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kwa juhudi kubwa walizozifanya kuokoa maisha ya watu. Amebainisha kuwa hadi sasa hakuna taarifa yoyote ya vifo iliyothibitishwa licha ya uharibifu mkubwa wa makazi ya wananchi.

Ameongeza kuwa baada ya kupokea taarifa za kuwepo kwa wananchi wasio na mahali pa kulala, ofisi yake ilichukua hatua za haraka kutafuta msaada wa magodoro, mablanketi pamoja na chakula ili kuhakikisha mahitaji muhimu yanapatikana kwa wakati.

Kwa upande mwingine, amesema ofisi ya mbunge imefanikiwa pia kupata unga ambao unatarajiwa kusambazwa kesho Jumamosi katika maeneo yaliyoathirika zaidi ikiwemo Ifakara, Lumemo na Michenga, ili kuwafariji na kuwasaidia wananchi waliokumbwa na adha hiyo.

Asenga amesisitiza kuwa wataendelea kuisimamia serikali kuhakikisha inatekeleza mipango ya kudhibiti athari za mafuriko, ikiwemo kufufua mabwawa, kupanua mito pamoja na kujenga miundombinu ya kinga kama matuta ili kupunguza madhara ya mafuriko siku zijazo.

Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa, takribani kaya 100 zenye jumla ya watu wapatao 500 zimeathirika na mafuriko hayo. Ingawa baadhi ya maeneo yameanza kupungua maji na wananchi kurejea makwao, bado wapo ambao hawajaweza kurudi kutokana na kiwango kikubwa cha maji kilichoingia kwenye makazi yao.

Kwa ujumla, juhudi za serikali zinaendelea kusaidia waathirika wa mafuriko katika Jimbo la Kilombero, huku msisitizo ukiwa ni kuhakikisha misaada ya dharura inawafikia wananchi wote walioathirika na kuweka mikakati madhubuti ya kudhibiti majanga kama haya siku zijazo.




NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) kwa kushirikiana na Tume ya Ushindani (FCC) wamekutana na wadau wa bidhaa za pombe nchini kwa lengo la kuwajengea uelewa juu ya matakwa ya sheria, kanuni na viwango vinavyosimamia sekta hiyo.

Kikao hicho kilichofanyika leo Machi 27, 2026 jijini Dar es Salaam, pia kimelenga kujadiliana na kubaini changamoto zinazowakabili wadau katika kukidhi matakwa ya kisheria pamoja na masuala ya ushindani, ili kupata ufumbuzi wake.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao hicho, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TBS, Mhandisi Yona Afrika, amesema kumekuwa na malalamiko yanayopokelewa na taasisi hizo kuhusu uwepo wa pombe duni na bandia katika soko, hali inayochangiwa na baadhi ya wafanyabiashara wasio waaminifu.

“Bidhaa hizi zisipozingatia matakwa yaliyowekwa, zinaweza kuhatarisha afya na usalama wa walaji,” amesema Afrika.

Ameongeza kuwa TBS kwa kushirikiana na FCC zitaendelea kuimarisha usimamizi wa viwango ili kudhibiti ubora wa bidhaa pamoja na kuhakikisha ushindani wa haki katika soko.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi.Roberta Feruzi, amesema uwepo wa pombe duni na bandia si tu unaharibu ushindani wa haki bali pia husababisha malalamiko kutoka kwa walaji kuhusu thamani ya fedha wanazolipa na athari za kiafya.

Amebainisha kuwa hali hiyo pia hudhoofisha biashara halali na kuvuruga mazingira ya ushindani sawa kwa wafanyabiashara wanaofuata sheria.








Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Wilaya ya Chamwino Mkoani Dodoma, limepanda zaidi ya miche ya miti elfu mbili ya vivuli pamoja na miche 420 ya matunda katika eneo lenye ukubwa wa heka tisa, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuunga mkono kampeni ya uhifadhi wa mazingira na kupambana na mabadiliko ya tabianchi.

Akizungumza Machi 27, 2026 wakati wa zoezi la upandaji miti,  lililofanyika katika eneo la ofisi za TANESCO wilayani humo, Mkuu wa Wilaya ya Chamwino, Mhe. Janeth Mayanja, amelipongeza shirika hilo kwa kuwa mstari wa mbele katika kuhamasisha upandaji miti kupitia kauli mbiu ya “Nitunze Nikutunze”.

Amesema wilaya hiyo imejiwekea lengo la kupanda miti laki mbili  katika kipindi hiki cha masika, ambapo miche tayari ipo katika vitalu vya Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Wilayani humo.

Aidha, amesema katika vijiji vyote 107 vya wilaya hiyo, miche ya miti elfu moja imegawiwa kwa kila kijiji na wananchi wamepewa bure ili kuipanda katika makazi yao na mashamba, hatua inayolenga kuongeza uoto wa asili na kuboresha mazingira.

Mhe. Mayanja ameongeza kuwa ndani ya miaka mitatu, eneo hilo linatarajiwa kuwa na miti mingi itakayosaidia kutoa kivuli, matunda pamoja na hewa safi kwa wananchi wanaofika kupata huduma mbalimbali kwenye ofisi hiyo.

Kwa upande wake, Meneja wa TANESCO Wilaya ya Chamwino, Mhandisi Judith Beatus, amesema zoezi hilo ni utekelezaji wa agizo la Rais Samia Suluhu Hassan la kuhimiza wananchi kushiriki kikamilifu katika utunzaji wa mazingira.

Naye mwakilishi wa Meneja wa TANESCO Mkoa wa Dodoma, James Vesso, amesema lengo la kupanda miti hiyo ni kuboresha mandhari ya Jiji la Dodoma na kuongeza kuwa shirika hilo limejipanga kuhakikisha miti yote iliyopandwa inalindwa na kukua vizuri.

Kipekee amemshukuru Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Lazaro Twange, kuwezesha zoezi hilo kwa kutenga rasilimali fedha, huku akisisitiza kuwa juhudi za upandaji miti zitaendelea kuwa endelevu ndani ya shirika hilo.

Kwa ujumla, juhudi hizi zinaonesha dhamira ya dhati ya TANESCO na Serikali katika kulinda mazingira, huku wananchi wakihimizwa kuendelea kushiriki kikamilifu katika upandaji na utunzaji wa miti kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.







 

 

Zaidi ya wanafunzi 400 wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi wamenufaika na huduma za bure za uchunguzi wa afya katika kambi maalum iliyoandaliwa na Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi Hesabu Tanzania (NBAA) kwa kushirikiana na Unique Group, ikiwa ni sehemu ya kurudisha kwa jamii katika maadhimisho ya miaka 30 ya kampuni hiyo.

Akizungumza wakati wa tukio hilo lililofanyika jijini Dar es Salaam siku ya Ijumaa, Mwenyekiti wa Bodi ya NBAA, CPA Prof. Sylivia Temu, alisema mpango huo unaonesha ushirikiano imara kati ya taasisi hizo mbili na kusisitiza umuhimu wa kuweka kipaumbele cha afya kwa vijana wanaojiandaa kufanya mitihani ya kitaaluma.

“Hatua hii inathibitisha ushirikiano wetu mzuri na Unique Group, kampuni inayotoa huduma za ukaguzi na uhasibu. Katika kuadhimisha miaka 30 tangu kuanzishwa kwake, wameamua kusherehekea kwa kuandaa kambi ya matibabu kwa gharama zao wenyewe kwa kushirikiana na Aga Khan Hospital,” alisema Temu.

Temu alibainisha kuwa lengo la kambi hiyo ni kutoa huduma za kinga kwa wanafunzi wanaojiandaa kufanya mitihani ya Bodi, akisisitiza kuwa afya njema ni msingi muhimu wa mafanikio ya kitaaluma na tija ya muda mrefu.

Alieleza kuwa uchunguzi huo unahusisha magonjwa mbalimbali ikiwemo matatizo ya macho, kisukari, saratani ya mlango wa kizazi pamoja na magonjwa ya zinaa. Aidha, waandaaji wameahidi kusaidia matibabu kwa hadi vijana 50 watakaobainika kuwa na changamoto za kiafya wakati wa zoezi hilo.

“Lengo kuu ni kuwakumbusha vijana kuwa afya yao ni muhimu katika kufanikisha malengo yao ya kitaaluma. Pia tumekuwa tukiwafikia kupitia majukwaa ya kidijitali, jambo linaloeleza mwitikio mkubwa tunaouona leo,” aliongeza, huku akiwahimiza vijana wengi zaidi kujiunga na taaluma ya uhasibu ambayo inalenga kulinda maslahi ya umma.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Unique Group, CPA Dr. B. S. Sree Kumar, alisema kambi hiyo ni sehemu ya uwajibikaji wa kampuni kwa jamii (CSR) katika kuadhimisha miaka 30 ya utoaji huduma.

“Tunapoadhimisha miaka 30, hii ni njia yetu ya kushukuru jamii. Tunarejesha kwa kushirikiana na NBAA, huku timu ya madaktari kutoka Aga Khan Hospital wakitoa huduma za uchunguzi wa afya ikiwemo sukari, macho, moyo, saratani ya matiti na matatizo mengine,” alisema Kumar.

Dk. Kumar alisisitiza kuwa kampuni hiyo iko tayari kusaidia wanafunzi watakaogundulika na matatizo ya afya wakati wa uchunguzi, akibainisha kuwa taasisi zinapaswa kurudisha kwa jamii kutokana na mchango wanaoupata.

Naye mwanafunzi wa CPA, Catherine Madembwe, alisema mpango huo umekuja kwa wakati muafaka na una manufaa makubwa, akibainisha kuwa vijana wengi hawana utaratibu wa kupima afya zao mara kwa mara.

“Tukio hili ni muhimu kwa sababu linatupa fursa ya kupima afya zetu ambayo mara nyingi hatupati. Nashauri kampuni nyingine ziige mfano huu kwa kuwa watu wengi hawana utamaduni wa kujichunguza afya zao, jambo linaloeleza mwitikio mkubwa unaoonekana,” alisema Madembwe.
Mwenyekiti wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) CPA Prof. Sylvia Temu akizungumza wakati wa ufunguzi wa huduma za bure za uchunguzi wa afya katika kambi maalum kwa wanafunzi wa mitihani ya uhasibu iliyoandaliwa na Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi Hesabu Tanzania (NBAA) kwa kushirikiana na Unique Group.
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania(​NBAA), CPA Pius A. Maneno akizungumza wakati wa ufunguzi wa huduma za bure za uchunguzi wa afya katika kambi maalum.
Mkurugenzi Mtendaji wa Unique Group, CPA Dr. B. S. Sree Kumar akizungumza kuhusu namna kampuni hiyo ilivyoweza kurudisha kwa jamii kwa kutoa huduma za bure za uchunguzi wa afya kwa wanafunzi wa wanaotegemea kufanya mitihani ya Bodi.
Wajumbe wa Bodi, watumishi wa NBAA pamoja na wanafunzi wa Mitihani ya Bodi wakifuatilia hotuba ya mgeni rasmi wakati wa ufunguzi wa huduma za bure za uchunguzi wa afya katika kambi maalum.
Huduma za uchunguzi wa afya ukiendelea

Top News