Serikali imevitaka vyama vya wafanyakazi nchini, ikiwemo Chama cha Walimu Tanzania (CWT), kutumia meza ya majadiliano (Social Dialogue) kutatua kero za wafanyakazi badala ya migongano isiyo na tija inayodhoofisha mshikamano na kushusha morali ya kazi.
Rai hiyo imetolewa na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi,Ajira na Mahusiano Mheshimiwa Dr. Evaline Munisi wakati akifungua rasmi mafunzo ya siku mbili kwa watumishi wa Makao Makuu na Makatibu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT) wa Mikoa na Wilaya kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi hiyo Deus Sangu leo Agosti 13, 2026 mjini Morogoro.
Amesema kuwa Vyama vya Wafanyakazi havikuundwa kwa ajili ya kusigana na Waajiri, bali viliundwa kama jukwaa la kisheria la kukaa meza moja na waajiri ili kujadiliana kwa hoja, ushahidi na kuheshimiana.
"Vyama vya wafanyakazi havikuundwa kwa ajili ya kusigana na waajiri, bali viliundwa kama jukwaa la kisheria la kukaa meza moja ili kupata suluhu ya pamoja. Katika miaka ya hivi karibuni tumeona kuibuka kwa makundi yanayojielekeza zaidi katika propaganda na migongano, jambo linalodhoofisha mshikamano wa walimu na kuathiri ubora wa elimu," alisema.
Akiangazia kaulimbiu ya CWT inayosema "Wajibu na Haki, Naibu Waziri amesema kuwa mambo hayo mawili ni kama ndugu pacha wanaotembea pamoja, hivyo ni lazima walimu watimize wajibu wao wa kiutumishi kabla ya kudai haki zao.
Amesema ni wajibu wa chama hicho kutetea maslahi ya walimu kama mishahara, upandaji vyeo na malimbikizo, lakini pia ni wajibu wao kuwasimamia walimu wafundishe kwa juhudi na nidhamu.
"Mwalimu asiyetimiza wajibu wake, anayetoroka kazini au anayekiuka maadili anakosa halali ya kimaadili ya kudai haki zake na anakiharibia chama sifa njema. Utendaji bora darasani ndio unaoipa CWT nguvu ya kusimama mbele ya Serikali kudai haki," alisema.
Ameongeza kuwa ulimwengu wa leo unaendeshwa na mifumo ya kidijitali na sheria, hivyo mtazamo wa zamani wa kuendesha vyama kwa mazoea na mihemko hauna nafasi tena, Serikali inatarajia kuona mabadiliko makubwa katika kasi ya kutatua kero za walimu na uadilifu wa matumizi ya fedha baada ya mafunzo hayo.
Katika hatua nyingine, Naibu Waziri amesema kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kufanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya elimu kwa kujenga miundombinu na kuajiri walimu wapya ili kupunguza mzigo wa kazi.
Aidha Serikali itaendelea kuweka mazingira bora ya kazi na kushirikiana na CWT ili kulinda amani na utulivu mahali pa kazi. Mafunzo hayo ya siku mbili yamejumuisha washiriki takriban 240 yakilenga kuwajengea uwezo katika sheria za kazi, taratibu za Tume ya Utumishi wa Walimu (TSC), na utendaji wa Bodi ya Kitaaluma ya Walimu.
Aikizungumza awali mwakilishi wa Msajili wa Vyama vya Wafanyakazi na Waajiri Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano Mussa Msami amesema kuwa kitengo cah Msajili wa Vyama vya Wafanyakazi na Waajiri milango iko wazi kwa ushauri ushirikiano wakati wote.
.jpeg)



.jpeg)


















.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)








.jpeg)


.jpeg)

.jpeg)








