Na.Mwandishi Wetu-Babati, Manyara

 Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) Kanda ya Kaskazini imeendesha semina ya kuwajengea uwezo Maafisa wa Huduma kwa Wateja, Mahusiano na Sheria kutoka TANESCO na Mamlaka za Majisafi na Usafi wa Mazingira za Kanda ya Kaskazini kuhusu huduma kwa wateja na uzingatiaji wa matakwa ya kisheria.

Akifungua semina hiyo katika Hoteli ya White Rose, Babati, Meneja wa EWURA Kanda ya Kaskazini, Bw. George Mhina, aliwasisitiza washiriki kuyafahamu vyema majukumu yao ili waweze kutoa majibu sahihi, ya wakati na yanayozingatia sheria, hivyo kuboresha huduma kwa wateja.

Kwa niaba ya washiriki, Bi. Devotha Mayala kutoka Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Tanga na Bw. Samwel Mandari kutoka TANESCO waliishukuru EWURA kwa mafunzo hayo, wakieleza kuwa yamewaongezea uelewa na uwezo wa kuwahudumia wateja kwa weledi zaidi.

Semina hiyo ni sehemu ya juhudi za EWURA za kuimarisha uwezo wa watoa huduma na kulinda haki za watumiaji wa huduma za nishati na maji kupitia Udhibiti wa Haki kwa Matokeo Chanya.

Mrajisi Msaidizi wa Vyama vya Ushirika Mkoa wa Dodoma, Joseph Chitinka, ameviagiza Vyama vya Msingi vya Ushirika (AMCOS) pamoja na Chama Kikuu cha Ushirika Mkoa wa Dodoma (DORECU) kuandaa mpango kabambe wa ununuzi wa mbegu bora za ufuta ifikapo Agosti 5, 2026, ili kuongeza ushindani wa mazao ya wakulima katika soko la kimataifa.

Akizungumza Julai 30, 2026, wakati wa kufunga mafunzo maalum ya siku tatu kwa viongozi wa AMCOS, wajumbe wa bodi na viongozi wa DORECU jijini Dodoma, Chitinka alisema Mkoa wa Dodoma umejipanga kuhamasisha uzalishaji wa ufuta mweupe wenye thamani kubwa sokoni badala ya kuendelea kutegemea aina za ufuta wa rangi zinazolimwa kwa wingi hivi sasa.

Aidha, aliwataka viongozi wa vyama vya ushirika kuhakikisha matumizi yote ya fedha yanaidhinishwa na maafisa ushirika pamoja na Ofisi ya Mrajisi, huku mikataba yote ya watoa huduma ikifuata taratibu za kisheria ili kuzuia vitendo vya udanganyifu na ubadhirifu wa fedha za wanachama.

Chitinka amesisitiza umuhimu wa kufuata sheria za manunuzi, kuandaa mipango ya kimkakati na kuhakikisha AMCOS zinafanya kazi mwaka mzima badala ya kuwa vyama vya msimu, amewahimiza viongozi kushirikiana na jamii kuongeza wanachama, kuimarisha uzalishaji wa mazao na kutumia kikamilifu mfumo wa stakabadhi za ghala.

Kuhusu uchaguzi wa viongozi wa ushirika, alisema ni wakati wa kutoa nafasi kwa viongozi wapya wenye sifa na kuacha mfumo wa viongozi kukaa madarakani kwa muda mrefu, ameeleza kuwa mchakato wa uchaguzi utaanza mwezi Agosti baada ya maadhimisho ya Nanenane.

Kwa upande wa usimamizi wa fedha, amesema matumizi yote ya fedha za mfumo wa stakabadhi za ghala yatapaswa kupitishwa kwenye bajeti za mwaka ili kuondoa mianya ya matumizi mabaya, amevitaka vyama vilivyoshiriki minada msimu uliopita kuhakikisha vinalipa tozo zote zinazodaiwa kwa wakati.

Naye Mrajisi Msaidizi kutoka Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC), Richard Izengo, amesema mafunzo hayo yamelenga kuimarisha usimamizi, ukaguzi na uwajibikaji wa vyama vya ushirika, amesisitiza umuhimu wa kuandaa hesabu na kuziwasilisha kwa mkaguzi wa nje ili kuongeza uwazi kwa wanachama.

Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa DORECU, David Mtimbi Mwaka, amesema mfumo wa stakabadhi za ghala Una matarajio ya mafanikio makubwa zaidi katika misimu ijayo, kufuatia kufanikiwa kwa kiasi kikubwa kuwadhibiti madalali wa mazao Mkoani Dodoma.





Chama Kikuu cha Ushirika Mkoa wa Dodoma (DORECU) kimefanikiwa kuuza zaidi ya tani 11,000 za ufuta na kuwalipa wakulima zaidi ya shilingi bilioni 25, huku kikitangaza kuwa kinajiandaa kuanza mauzo ya mazao ya pamba na dengu hivi karibuni.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kuhitimisha mafunzo ya siku tatu kwa wanaushirika 80 kutoka wilaya mbalimbali za Mkoa wa Dodoma, Meneja Mkuu wa DORECU, Feruzi Hassan Mwindi, alisema mafunzo hayo yalilenga kufanya tathmini ya utekelezaji wa mfumo wa stakabadhi za ghala kwa msimu uliopita, kuimarisha utunzaji wa kumbukumbu na kuwajengea uwezo viongozi wa vyama vya ushirika katika usimamizi wa shughuli zao.

Mwindi alisema mafunzo hayo yatawanufaisha wakulima wengi ambao ni wageni katika matumizi ya mfumo wa stakabadhi za ghala, kwa kuwa yatawawezesha kuhifadhi kumbukumbu na takwimu kwa usahihi pamoja na kuendesha vyama vyao kwa ufanisi zaidi katika misimu ijayo.

Makamu Mwenyekiti wa DORECU, David Mtimbi Mwaka, alisema wanachama wa mkoa wa Dodoma wamenufaika na mfumo wa stakabadhi za ghala ambao umechangia kudhibiti madalali (aggregators), akieleza kuwa mafanikio yaliyopatikana yanatoa matumaini ya kufanya vizuri zaidi katika msimu ujao.

Naye Mrajisi Msaidizi anayesimamia vyama vya ushirika visivyo vya kifedha kutoka Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC), Richard Izengo, alisema mafunzo hayo ni sehemu ya utaratibu wa kila mwaka wa kuimarisha usimamizi na ukaguzi wa vyama vya ushirika.

Pia alisisitiza umuhimu wa kuandaa na kuwasilisha hesabu kwa mkaguzi wa nje ili taarifa za utekelezaji wa shughuli za vyama ziwasilishwe kwenye mikutano mikuu ya mwaka na kuongeza uwajibikaji kwa viongozi na wanachama.







MAHAKAMA ya Rufani Tanzania imetupilia mbali ombi la Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) lililotaka kuruhusiwa kuwasilisha ushahidi wa nyongeza katika kesi ya uhaini inayomkabili Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Tundu Lissu, na hivyo kuacha uamuzi wa Mahakama Kuu ukiwa palepale.

Uamuzi huo ulitolewa na jopo la majaji watatu wa Mahakama ya Rufani lililoundwa na Jaji Augustine Mwarija, Jaji Zahara Muruke na Jaji Amour Khamisi, ambao walikubaliana na uamuzi wa awali wa Mahakama Kuu uliotolewa na Jaji Dunstan Ndunguru, akisaidiana na Majaji James Karayemaha na Ferdinand Kiwonde.

Akisoma hukumu, Jaji Mwarija alisema hoja kuu ilikuwa kubaini kama Mahakama Kuu ilikosea kwa kujadili na kukataa notisi ya ushahidi wa nyongeza bila kuipa Jamhuri nafasi ya kusikilizwa, lakini Mahakama ya Rufani ilibaini kuwa upande wa mashtaka ulipewa fursa ya kutosha kueleza msimamo wake.

Mahakama ilieleza kuwa notisi ya Jamhuri ililenga kuongeza maelezo ya ushahidi wa ACP Amini Mahamba kuhusu uchunguzi wa matukio ya Oktoba 29, 2025, maelezo ambayo hayakusomwa wakati wa mwenendo wa kupeleka shauri Mahakama Kuu (committal proceedings).

Hata hivyo, Lissu alipinga hatua hiyo akidai kuwa kifungu cha 308 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai hakiruhusu kuwasilishwa kwa ushahidi mpya kutoka kwa shahidi ambaye tayari ushahidi wake ulishawasilishwa wakati wa committal, bali kinahusu mashahidi ambao taarifa zao hazikusomwa kabisa.

Mahakama ya Rufani ilikubaliana na tafsiri hiyo, ikisema kifungu hicho kinatoa nafasi ya kumwita shahidi ambaye taarifa yake haikusomwa wakati wa committal, lakini hakitoi mamlaka ya kumrejesha shahidi aliyekwisha kutoa ushahidi ili kuongeza ushahidi mpya alioupata baadaye.

Kutokana na tafsiri hiyo, Mahakama ilisema notisi ya Jamhuri ilikuwa imewasilishwa kwa msingi usio sahihi wa kisheria na kwamba Mahakama Kuu ilikuwa sahihi kuifuta kwa kuwa haikukidhi matakwa ya kifungu cha 308 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai.

Katika uamuzi huo, Mahakama pia ilikataa ombi la Lissu la kulipwa fidia kwa madai ya kukaa mahabusu kwa siku 139 kutokana na kusimamishwa kwa mwenendo wa kesi wakati maombi hayo yalipokuwa yakisikilizwa.

Jaji Mwarija alisema Mahakama ya Rufani haina mamlaka ya kushughulikia ombi hilo kwa kuwa si Mahakama ya kwanza kusikiliza shauri, akifafanua kuwa fidia ya aina hiyo inaweza kutolewa tu endapo mshtakiwa ataachiwa huru na kubainika kuwa shtaka lilikuwa la kipuuzi au la kumsumbua bila sababu.

Kutokana na sababu hizo, Mahakama ya Rufani ilihitimisha kuwa ombi la DPP halikuwa na msingi wa kisheria na hivyo likatupiliwa mbali, hatua inayomaanisha uamuzi wa Mahakama Kuu wa kuzuia kuwasilishwa kwa ushahidi huo wa nyongeza unabaki kuwa halali.

Na Janeth Raphael - MichuziTv

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema Serikali itaendelea kuimarisha maridhiano ya kisiasa kama msingi wa kuendeleza mchakato wa maboresho ya Katiba, huku akisisitiza kuwa hatua zote zitafanyika kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za nchi kwa maslahi mapana ya Taifa.

Rais Samia ametoa kauli hiyo leo Julai 30, 2026, alipokutana na viongozi wa vyama 18 vya siasa nchini katika Ikulu ya Dar es Salaam, kwenye mkutano uliolenga kujadili masuala ya maridhiano ya kisiasa, mageuzi ya kisiasa, uchumi, huduma za jamii, ajira, uwekezaji na ulinzi wa amani nchini.

Akizungumza katika mkutano huo, Rais Samia alisema Serikali imejipanga kuendelea kushirikiana na vyama vya siasa ili kuhakikisha mchakato wa maridhiano unazaa matokeo yenye manufaa kwa Taifa, ikiwa ni pamoja na kufungua njia kuelekea hatua zinazofuata za maboresho ya Katiba.

Aidha, amewafahamisha viongozi hao kuhusu hatua zilizofikiwa katika maandalizi ya mchakato wa maridhiano visiwani Zanzibar, akieleza kuwa Serikali itaendelea kusimamia mchakato huo kwa uwazi na kwa kuzingatia misingi ya kisheria.

Rais Samia pia alitangaza kuwa Serikali itaendelea kufanya mikutano ya mazungumzo na viongozi wa vyama vya siasa angalau mara tatu kwa mwaka, akisema hatua hiyo inalenga kuimarisha ushirikiano, kujenga uelewano na kutatua changamoto mbalimbali kupitia majadiliano.

Mbali na masuala ya kisiasa, Rais Samia alielezea hali ya uchumi wa nchi, akisema Tanzania imeendelea kushuhudia ukuaji wa uchumi wa asilimia sita katika mwaka uliopita, huku ukuaji wa asilimia 6.3 ukitarajiwa kufikiwa mwaka huu.

Amesema Serikali inaendelea kuweka mkazo katika kukamilisha miradi mikubwa ya maendeleo iliyoanza kutekelezwa pamoja na kuwekeza zaidi katika miundombinu ya kimkakati, ikiwemo reli, barabara, bandari na sekta nyingine muhimu kwa maendeleo ya uchumi.

Kuhusu uwekezaji, Rais Samia alisema maboresho yaliyofanyika katika Bandari ya Dar es Salaam yameongeza uwezo wa bandari hiyo kuhudumia biashara ya ndani na kikanda, huku Serikali ikiendelea kupanua na kuboresha shughuli za bandari za Bahari ya Hindi pamoja na zile za maziwa ya Victoria, Tanganyika na Nyasa.

Aidha, amewataka viongozi wa vyama vya siasa kushirikiana katika kulinda amani, umoja na maslahi ya Taifa, akisisitiza kuwa ulinzi wa Tanzania ni jukumu la pamoja linalohusisha Serikali, vyama vya siasa na wananchi wote.

Katika mkutano huo, viongozi wa vyama vya siasa waliwasilisha maoni na mapendekezo yao kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu maendeleo ya kisiasa, kijamii na kiuchumi. Serikali iliahidi kuendelea kuyapokea na kuyafanyia kazi kupitia majukwaa rasmi ya majadiliano na mifumo ya maamuzi.

Mkutano huo ni wa pili kuitishwa na Rais Samia tangu kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025. Mkutano wa kwanza ulifanyika Machi 31, 2026, Ikulu ya Dar es Salaam, ukiwakutanisha wagombea wa urais na wagombea wenza kutoka vyama vya siasa vilivyoshiriki uchaguzi huo.






Na Janeth Raphael - MichuziTv

Watendaji wa Serikali za Mitaa nchini wamehimizwa kutenganisha majukumu yao ya kiutumishi na shughuli za kisiasa ili kulinda weledi, uadilifu na kutenda haki kwa wananchi, hatua itakayosaidia kuimarisha imani ya umma kwa Serikali pamoja na kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma.

Wito huo umetolewa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Watendaji wa Serikali za Mitaa Tanzania (UWATA), Frank Kalinga, wakati wa uzinduzi rasmi wa umoja huo uliofanyika jijini Dodoma.

Kalinga amesema hadhi na heshima ya watendaji wa Serikali za Mitaa inategemea namna wanavyotekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria, kanuni na maadili ya utumishi wa umma, huku wakiepuka kuchanganya wajibu wao wa kitaaluma na shughuli za kisiasa.

Amesisitiza kuwa watendaji ni kiungo muhimu kati ya Serikali na wananchi katika ngazi za msingi, hivyo wanapaswa kujenga mazingira ya kuaminika kupitia utendaji wenye uwazi, uwajibikaji na usio na upendeleo.

"Ni muhimu kila mdau kuheshimu mipaka ya mamlaka na majukumu yaliyoainishwa kisheria ili kuimarisha uwajibikaji na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi," amesema Kalinga.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais – TAMISEMI, Sospeter Mtwale, amesema kuanzishwa kwa UWATA ni hatua muhimu itakayosaidia kuimarisha uwezo wa watendaji wa Serikali za Mitaa, kukuza maadili ya utumishi wa umma na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa sera pamoja na miradi ya maendeleo katika ngazi za kata, vijiji na mitaa.

Mtwale amewataka watendaji kuendelea kuzingatia misingi ya utawala bora, uzalendo, uwajibikaji na usimamizi makini wa rasilimali za umma ili kuhakikisha miradi ya maendeleo inatekelezwa kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa.

Ameeleza kuwa watendaji wana nafasi ya kipekee katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na kwamba usimamizi madhubuti wa miradi ya maendeleo utachangia kuleta matokeo chanya, kuongeza thamani ya fedha za umma na kuharakisha maendeleo katika jamii.











NA: MWANDISHI WETU


Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Taifa, na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu (MCC), Mary Chatanda, amebadilishwa mkoa wa ulezi wa kichama na sasa ni mlezi wa CCM mkoa wa Mara.

Mabadiliko hayo yamefanyika Julai 29, 2026, Zanzibar, kufuatia vikao vya Chama vinavyoendelea. Kabla ya mabadiliko hayo, Chatanda alikuwa mlezi wa mikoa ya Mjini na Magharibi, Zanzibar.

Akizungumzia mabadiliko hayo, Chatanda amekishukuru Chama chake kwa kuendelea kumuamini kutekeleza majukumu mbalimbali ya kichama.

"Nimepokea taarifa hii ya mabadiliko ya ulezi wa Chama mkoa kwa moyo wa unyeyekevu. Nakishukuru Chama changu kwa kuniamini. Niwaombe wanachama wenzangu na wananchi kwa ujumla tushirikiane kuhakikisha tunasukuma mbele gurudumu la maendeleo na Chama chetu".

Ameongeza kuwa "Serikali ya CCM chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan imepeleka fedha nyingi za miradi ya maendeleo mkoani Mara, ni wajibu wetu kuhakikisha fedha hizo zinatumika kama ilivyokusudiwa katika kuboresha maisha ya wananchi". 

Akiwa mlezi mkoani humo, pamoja na mambo mengine, Chatanda anawajibika kuwaunganisha wanachama wa CCM na wananchi kwa ujumla.

Aidha, kuimarisha uhai wa Chama, kuongeza idadi ya wanachama na kuhimiza utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ili kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Vilevile, anawajibika kujenga uhusiano mzuri baina ya Chama na serikali.

Mkoa wa Mara unaundwa na wilaya za Bunda, Butiama, Musoma, Rorya, Serengeti na Tarime.



Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Mjumbe wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) na Kaimu Meneja wa Huduma za Kiswahili wa Shirika la Magazeti ya Serikali (TSN), Mgaya Kingoba, amesema uhuru wa kutoa maoni una mipaka ya kisheria na kimaadili, hivyo haupaswi kutumiwa kutoa matusi, kudhalilisha wengine, kuchochea chuki au kusambaza taarifa zisizo sahihi.

Kingoba amesema hayo leo, Julai 30, 2026, alipowasilisha mada kuhusu “Kuimarisha Uzalendo katika Uandishi wa Habari ili Kulinda Amani, Umoja na Mshikamano” katika siku ya pili ya mafunzo kwa watumishi wa Bongo FM, redio dada ya TBC (Shirika la Utangazaji Tanzania), yaliyofanyika katika Ofisi za JAB jijini Dar es Salaam kuanzia Julai 29, 2026.

Amesema ukosoaji ni sehemu muhimu ya uhuru wa kujieleza, lakini unapaswa kulenga kuonesha kasoro na kuchochea maboresho badala ya kushambulia watu, kutumia lugha ya kejeli au kubomoa imani ya jamii kwa taasisi.

“Mkosoaji mzalendo hafichi makosa, lakini pia hatumii matusi, kejeli au upotoshaji. Anakosoa kwa ukweli, ushahidi na lugha ya staha, akiwa na lengo la kujenga na kuboresha,” amesema Kingoba.

Ameeleza kuwa mkosoaji mzalendo hujenga ukosoaji wake katika misingi ya ukweli, ushahidi, muktadha, lugha ya staha, maslahi ya umma na mapendekezo ya suluhisho.

Aidha, amewataka watangazaji kutambua kuwa uhuru wa kujieleza hauondoi wajibu wao wa kulinda utu wa watu, amani na mshikamano wa kitaifa.

Kingoba amesema uzalendo katika utangazaji hauishii katika kuipenda nchi kwa maneno, bali unapaswa kuonekana katika maamuzi ya kitaaluma yanayolinda ukweli, umoja, amani na maslahi ya Taifa na kwamba uchaguzi wa maneno na namna ya kuendesha mijadala ya moja kwa moja unaweza kujenga jamii au kusababisha migawanyiko.

Akiwasilisha mada kuhusu Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, amesema Sheria hiyo inatambua uhuru wa Waandishi wa Habari na vyombo vya habari katika kutafuta, kuhariri, kuchapisha na kutangaza habari, lakini inaweka pia wajibu wa kuzingatia sheria, maadili, weledi na haki za wengine.

Amesema uhuru wa habari na uwajibikaji vinapaswa kwenda pamoja ili kulinda taaluma, maslahi ya jamii na Taifa.

Mafunzo hayo yanalenga kuwaongezea washiriki uelewa kuhusu Sheria ya Huduma za Habari, maadili ya uandishi wa habari, uzalendo na wajibu wa watangazaji katika kutumia uhuru wa kujieleza kwa weledi na uwajibikaji.













Na George Maziku, Nyang'hwale


MGODI wa wachimbaji wadogo wa dhahabu wa Mwamakiliga, unaopatikana Kijiji cha Mwamakiliga, kata ya Izunya, wilaya ya Nyang'hwale, Mkoani Geita umewawezesha zaidi ya watanzania 6000 kujiajiri kwenye kazi mbalimbali mgodini hapo na kujipatia kipato.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mgodini hapo, Meneja msaidizi wa mgodi huo Mashaka Kulwa Chitela amesema wananchi kutoka ndani na nje ya wilaya ya Nyang'hwale na mkoa wa Geita wamenufaika kwa kujipatia kazi mbalimbali.

Amesema kuwa wananchi hao wanajishughulisha na kazi za uchimbaji, uokotaji wa mawe ya dhahabu(maarufu ukwale), biashara ya mitambo ya kusaga mawe (crushers), ubebaji wa mifuko ya mawe, boda boda, mama lishe, biashara ya nyumba za kupangisha, maduka, na nyingine nyingi.

"Mgodi wetu umeisaidia sana serikali katika kupunguza idadi ya watanzania wasio na ajira, hapa kuna umati wa zaidi ya watu 6000 wanaojipatia riziki zao za Kila siku. Wapo wachimbaji, kina mama wa ukwale, makago wanaobeba na kupakia mifuko ya mawe, boda boda, mama lishe, wenye gesti, maduka na wafanyabiashara wengine wengi", amesema Chitela.

Ameongeza kuwa, "Tumetengeneza ajira za uhakika zaidi ya 100 katika kada za ukaguzi, ulinzi, ulipuaji na uhudumu wa ofisi. Tuna imani kubwa kwamba tukipata leseni ya uchimbaji tutazalisha ajira Nyingi zaidi."

Amebainisha miongoni mwa watu walionufaika na mgodi huo ni wakazi wa kijiji cha Mwamakiliga na kata ya Izunya ambao wamekuwa wakipewa kipaumbele katikà nafasi mbalimbali za kazi zinazojitokeza mgodini hapo.

" Tumekuwa na upendeleo maalum kwa wananchi wa kijiji hiki ambao ni wenyeji wetu, walinzi wengi wa mgodi wetu wanatoka hapa Mwamakiliga. Pia tumechukua vijana 25 wa hapa kijijini na Kisha kuwafundisha kazi ya ukaguzi wa migodi", amesitiza Chitela.

Amefafanua mbali na kuzalisha ajira hizo, mgodi wake umekuwa chanzo cha uhakika cha mapato ya halmashauri ya wilaya ya Nyang'hwale kupitia ushuru mbalimbali ikiwemo ushuru wa huduma.

Amesema hata Serikali kuu imekuwa ikinufaika na uwepo wa mgodi huo kupitia malipo ya mrabaha, ambayo ni asilimia 3 kwa kila mifuko 100 ya mawe yenye dhahabu.

"Serikali imetuamini na kutukabidhi jukumu la kusimamia na kukusanya mapato yake katika mgodi huu, kazi hiyo tumekuwa tukiifanya kwa uaminifu mkubwa. Halmashauri yetu ya Nyang'hwale na serikali kuu wote wanapata mapato yao bila ubabaishaji", amebainisha Chitela.

Kuhusu usalama wa mgodi wake kwa wachimbaji na watu wengine wanaofanya kazi mgodini hapo, Chitela amesema suala la usalama kwao ni kipaumbele namba moja, na kwamba mgodi huo haujawahi kupata ajali yoyote kubwa kutokana na umakini wao mkubwa katika usalama.

"Mgodi wetu ni salama kabisa, kwetu suala la usalama ni kipaumbele cha kwanza na idara yetu ya ukaguzi ina watu wa kutosha na makini. Ukaguzi wa duara unafanyika wakati wote mchana na usiku, masaa 24 na mara ikibainila kama duara fulani ni hatarishi, tunasimamisha moja uchimbaji mpaka marekebisho yafanyike",amesema.






Victor Masangu,Bagamoyo


Mwenyekiti wa Jumuiya ya ya Wazazi Taifa Ndg. Fadhili Maganya amewasa viongozi wa CCM kuhakikisha kwamba wanavalia njuga na kusimamia ipasavyo suala la mikopo ya asilimia kumi ambayo inatolewa na Halmashauri.

Kauli hiyo ameitoa wakati wa ziara yake ya kikazi Wilaya ya Bagamoyo yenye lengo la kuona uhai wa chama pamoja na kuimarisha jumuiya zake zote sambamba na tenbelea miradi ya maendeleo.

Mwenyekiti huyo amebainisha kwamba kumekuwepo na baadhi changamoto ya utoaji wa fedha ambazo zinatolewa na mfuko wa Tasaf aziwafikii walengwa na zinakwenda kwa watu wengine ambao hawastahili

"Kuna malalamiko mengi ambayo yamekuwa yakitolewa na wananchi kuhusiana na suala la utoaji wa fedha ambazo zinatolewa na mfuko wa Tasaf zinakwenda kwa watu wengine ambao hawahusiki kabisa,"amebainisha Mwenyekiti huyo.

Kadhalika amesema kwamba fedha za asilimia kumi ambazo zinatolewa kwa ajili ya makundi ya vijana,walemavu na wanawake zinatakiwa kutolewa kwa walengwa na sio kupewa watu wengine.

Akiwa katika chuo cha uuguzi na ukunga Mwenyekiti huyo amewahimiza wanafunzi hao kuzingatia maadili pamoja na kuwa wazalendo na nchi yao.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo Shaibu Ndemanga amempongeza Mwenyekiti huyo wa Taifa kwa kufanya ziara hiyo ambayo itaweza kuleta matokeo chanya ya kimaendeleo.

Pia Mkuu huyo wa Wiaya amebainisha kuwa serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 27 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbali mbali ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa bandari.

Naye Mwenyekiti wa chama cha mapinduzi (CCM) Wilaya ya Bagamoyo Abubakari Mlawa amebainisha kwamba bado kuna changamoto ya migogoro ya ardhi katika baadhi ya maeneo na kwamba wameshaanza kuifanyia kazi.

Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo Subira Mgalu ameamua kutoa kiasi cha shilingi milioni 5 kupitia mfuko wa Jimbo kwa ajili ya kuweza kukarabati miundombinu ya majengo pamoja na uzio katika chuo cha uuguzi na ukunga Bagamoyo.

Mwenyekiti wa wazazi Mkoa wa Pwani Jackson KItuka amesema wataendelea kushirikiana na viongozi mbali mbali wa chama na serikali kwa ajili ya kuleta maendeleo.

Ziara ya Mwenyekiti wa Jumuiya ya wazazi ya CCM Taifa imeendelea katika Wilaya ya Bagamoyo ambapo imetembelea miradi mbali mbali ya maendelo ikiwemo chuo cha uuguzi na ukunga,chuo cha kilimo kaole,kiwanda cha kuchakata taka hatarishi pamoja na miradi mbali ikiwemo Hospitali ya Chalinze na sekta ya elimu.




Top News