Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Ndg. Abdi Mahmoud Abdi, amesema CCM itaendelea kuboresha mazingira na huduma za kazi kwa watumishi wa Chama hicho, kwa lengo la kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao.

Ndg. Abdi ameyasema hayo leo, Septemba 13, 2026, alipowasili katika Tawi la CCM Kivunge A, Jimbo la Kijini, ambapo amefurahishwa na hali ya uhai, umoja na mshikamano miongoni mwa wanachama wa CCM katika jimbo hilo.

Amesema hali hiyo ni ishara ya mshikamano wa wanachama, jambo alilolitaja kuwa ni msingi muhimu katika kukiimarisha Chama na kufanikisha utekelezaji wa majukumu yake.

Kwa upande wake, Katibu wa NEC, Idara ya Itikadi na Uenezi, Ndg. Khamis Mbeto Khamis, amesema ziara hiyo inalenga kukagua na kutathmini hali ya uhai wa CCM kuanzia ngazi ya matawi hadi jimbo.

Aidha, amewataka wanachama wa CCM kuelekea uchaguzi wa ndani wa Chama mwaka 2027 kutumia fursa hiyo kuchagua viongozi bora, wenye uwezo wa kukiongoza Chama na kukivusha kwa mafanikio kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2030.

Katika ziara hiyo, Ndg. Abdi pia amemtembelea na kumjulia hali Ndg. Khamis Ali Khamis nyumbani kwake Kivunge B, hatua aliyosema inalenga kuendelea kuonesha thamani ya kuwajali, kuwathamini na kuwakumbuka wazee pamoja na wanachama waliokitumikia Chama Cha Mapinduzi.








Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Ndg. Abdi Mahmoud Abdi, amesema changamoto zinazowakabili wananchi zinapaswa kutatuliwa kuanzia katika ngazi zote za maamuzi ndani ya Chama, kuanzia matawi hadi Afisi Kuu ya CCM.

Ndg. Abdi ameyasema hayo leo, Septemba 13, 2026, alipowasili katika Tawi la CCM Kivunge, Jimbo la Kijini, ambapo alizungumza na wanachama wa CCM pamoja na wajumbe wa Kamati za Siasa.

Amesema ushiriki wa wanachama katika vikao mbalimbali vya Chama ni muhimu katika kuimarisha umoja na mshikamano kati ya viongozi na wanachama, sambamba na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya Chama.

Aidha, amesema Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar, ambaye pia ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, anaendelea kutekeleza Ilani ya CCM kwa vitendo, ikiwemo kuhakikisha wananchi wanapata ufumbuzi wa changamoto zinazohusu huduma za kijamii.

Amezitaja huduma hizo kuwa ni pamoja na elimu, afya, maji safi na salama, pamoja na ujenzi na uboreshaji wa miundombinu ya barabara.

Katika ziara hiyo, Ndg. Abdi pia alimtembelea na kumjulia hali Ndg. Fatima Mtwana Ame nyumbani kwake Kivunge, akisisitiza umuhimu wa kuendeleza mshikamano, upendo na kujali wanachama wa CCM.










Na. Vero Ignatus, Michuzi TV – Arusha

​Tanzania imesisitiza umuhimu wa kuimarisha huduma za afya ya msingi ili kufikia huduma bora za afya kwa wote huku ikiweka mkazo katika uwekezaji, upatikanaji wa fedha, matumizi ya teknolojia, na kuhakikisha usawa katika utoaji wa huduma hizo nchini.

​Akifunga Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Huduma za Afya ya Msingi (IPHC2026) kwa niaba ya Waziri wa TAMISEMI Prof. Shemdoe, Naibu Waziri Dkt. Festo Dugange amesema jitihada za Serikali katika kuimarisha afya ya msingi na hospitali za rufaa zimeiwezesha Tanzania kutambulika zaidi barani Afrika.

​Dkt. Dugange ameeleza kuwa hatua hizo kubwa zimesaidia kupunguza vifo vya wanawake vitokanavyo na uzazi kutoka vifo 556 mwaka 2015/2016 hadi vifo 104 kwa kila vizazi hai laki moja,Aidha, nchi za Afrika zimehimizwa kujenga mifumo inayostahimili mabadiliko ya tabianchi na kuendeleza ajenda ya Three Zeros.

​Aliongeza kuwa uwekezaji katika sekta ya afya lazima uambatane na mnyororo imara wa ugavi wa bidhaa, watumishi wenye ujuzi, dawa, vifaa tiba, na mifumo ya kidijitali. Hatua hii itasaidia taasisi za afya kubadilishana taarifa na kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma kwa wananchi.

​Mkutano huo umefikia maazimio 10, yakiwemo kuzitaka Serikali za Afrika kuweka afya ya msingi kuwa kipaumbele kwenye bajeti zao. Lengo ni kuongeza fedha za ndani ili wananchi wapate huduma bora, nafuu, na kwa wakati bila kujali maeneo wanayotoka au uwezo wao kiuchumi.

​Pia imesisitizwa kuwa kuimarisha afya ya msingi pamoja na hospitali za mikoa, kanda, na taifa utaongeza uwezo wa mfumo wa afya na kupunguza changamoto za huduma vijijini, ambapo washiriki wanetakiwa kuhakikisha maazimio yote yanatekelezwa kwa vitendo baada ya kurejea makwao.

​Katika hatua nyingine, Dkt. Dugange amesisitiza kila mwananchi apate huduma bila ubaguzi wowote. Ametaka kuimarishwa kwa mifumo ya kidijitali ya taarifa za afya, bima, na ufuatiliaji wa magonjwa ili kuboresha utendaji kazi katika sekta hiyo.

​Maazimio mengine ni pamoja na kuimarisha ufadhili unaozingatia utendaji (performance-based financing), kutekeleza ajenda ya Lusaka, kutumia tafiti kwenye maamuzi, kuendeleza watumishi wa afya, na kuwekeza kwenye malezi ya mtoto kupitia African Union Champion Roadmap on Nurturing Care.









Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Ndg. Abdi Mahmoud Abdi, amesema CCM itaendelea kuimarisha uhai na uimara wa chama, ikiwemo kujenga na kuimarisha matawi yake katika majimbo mbalimbali.

Ndg. Abdi ameyasema hayo alipowasili katika Tawi la CCM Kidagoni, Jimbo la Nungwi, ikiwa ni sehemu ya mwendelezo wa ziara zake za kukagua na kuimarisha uhai wa CCM kuanzia ngazi ya matawi hadi majimbo.

Amesema uhai na uimara wa chama unategemea kwa kiasi kikubwa ushiriki wa wanachama wake katika kutekeleza wajibu wao, hususan kulipa ada za uanachama kwa wakati, ambazo huchangia katika utekelezaji wa shughuli mbalimbali za chama, ikiwemo ujenzi na uimarishaji wa matawi.

Aidha, Ndg. Abdi amesema amezipokea changamoto zilizowasilishwa na viongozi pamoja na wanachama wa Tawi la CCM Kidagoni, zikiwemo ukosefu wa jengo la tawi kwa ajili ya shughuli za chama na changamoto ya miundombinu ya barabara.

Amesisitiza kuwa uongozi wa CCM utaendelea kuzifuatilia changamoto hizo kwa lengo la kuboresha mazingira ya utendaji wa chama na kuwawezesha viongozi na wanachama kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Katika ziara hiyo, Ndg. Abdi pia alipata fursa ya kumtembelea na kumjulia hali Ndg. Asiata Hamada Suleiman nyumbani kwake Kidagoni.








Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Ndg. Abdi Mahmoud Abdi, amewasili katika Tawi la CCM Kidoti, Jimbo la Nungwi, na kufanya mazungumzo na viongozi pamoja na wanachama wa chama hicho.

Ziara hiyo ni sehemu ya mwendelezo wa ukaguzi wa uhai wa CCM unaofanyika kuanzia ngazi ya matawi hadi majimbo, kwa lengo la kuimarisha chama na kuhakikisha shughuli zake zinatekelezwa kwa ufanisi.

Akizungumza na wanaCCM hao, Ndg. Abdi amewataka wanachama kuendelea kulipa ada zao za uanachama kwa wakati, akisisitiza kuwa ulipaji wa ada ni miongoni mwa wajibu muhimu unaochangia kukifanya chama kuwa imara na hai.

Amesema ushiriki wa wanachama katika kutekeleza wajibu wao utasaidia kuongeza uwezo wa CCM kutekeleza kwa vitendo Ilani ya Uchaguzi ya chama hicho na kusimamia utekelezaji wa ahadi zake kwa wananchi.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa viongozi na wanachama kuendelea kushirikiana, kusikilizana na kudumisha mshikamano ili kuongeza ufanisi wa shughuli za chama katika ngazi zote.

Kwa upande wake, Katibu wa Kamati Maalum wa Idara ya Oganaizesheni CCM Zanzibar, Ndg. Omar Ibrahim Kilupi, amewataka wanaCCM kuendelea kujiandikisha na kupata Kitambulisho cha Mzanzibari Mkazi, hatua itakayowawezesha kujiandaa kutimiza haki yao ya msingi ya kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2030.

Ndg. Abdi anaendelea na ziara yake katika maeneo mbalimbali kwa ajili ya kukagua uhai wa CCM, huku akikutana na viongozi na wanachama kwa lengo la kusikiliza changamoto zao, kuimarisha mshikamano na kuongeza ufanisi wa shughuli za chama.








Wakulima wa kahawa Tanzania wanaonufaika na programu za Taasisi ya Hanns R. Neumann Stiftung (HRNS) wameondolewa hofu kufuatia mabadiliko ya uongozi katika taasisi hiyo, huku uongozi ukisisitiza kuwa mabadiliko hayo hayataleta mabadiliko katika dhamira yake ya kusaidia wakulima, bali yataimarisha zaidi kazi hiyo.

Kuanzia Oktoba 1, 2026, Michael R. Neumann ataachia nafasi ya Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya HRNS baada ya zaidi ya miongo miwili, na nafasi hiyo kuchukuliwa na Dkt. Nina Smidt, mtendaji mwenye uzoefu wa kimataifa katika uendeshaji wa taasisi za kijamii, ambaye pia ni Mkurugenzi Mtendaji na Msemaji wa Bodi ya Siemens Stiftung.

HRNS, yenye makao yake nchini Ujerumani na inayosaidia jamii zinazolima kahawa, imekuwa ikifanya kazi na wakulima Tanzania tangu mwaka 2006. Mabadiliko hayo yanakuja wakati wakulima wakikabiliwa na changamoto zinazoongezeka, zikiwemo mabadiliko ya tabianchi, kupanda kwa gharama za uzalishaji na haja ya fursa endelevu zaidi za kiuchumi.

Meneja wa HRNS Tanzania, Morgan Mkonyi, amesema mabadiliko hayo yatajengwa juu ya kazi iliyofanywa na taasisi hiyo badala ya kubadili msingi wa dhamira yake.

“Mchango wa Michael R. Neumann katika ukuaji na maendeleo ya HRNS umeweka msingi imara ambao tunaweza kuendelea kuujengea. Tunapomkaribisha Dkt. Nina Smidt kama Mwenyekiti mpya, tunaona mabadiliko haya si kama kuachana na dhamira yetu, bali kama fursa ya kuiimarisha na kuisogeza mbele zaidi,” alisema.

Mkonyi alisema HRNS imepanua wigo wa kazi zake kutoka kuongeza uzalishaji wa kahawa pekee hadi kushughulikia mazingira mapana yanayoamua ustawi endelevu wa wakulima na familia zao.

Kwa sasa, programu za HRNS zinajumuisha kilimo kinachozingatia mabadiliko ya tabianchi, agroforestry, ulinzi wa mazingira, fursa za kiuchumi kwa vijana na kuimarisha mashirika ya wakulima, sambamba na juhudi za kuongeza uzalishaji wa kahawa.

“Kilimo kinachozingatia mabadiliko ya tabianchi pamoja na agroforestry kinaweza kuwasaidia wakulima kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa huku wakilinda rutuba ya udongo na vyanzo vya maji,” alisema Mkonyi.

Alisema kuimarika kwa mashirika ya wakulima kunaweza kuongeza uwezo wao wa kupata huduma, maarifa na masoko, huku programu za vijana zikilenga kujenga fursa mpya za kiuchumi kwa kizazi kijacho. HRNS pia imekuwa ikichunguza miradi ya kaboni inayounganisha uzalishaji wa kilimo na uhifadhi wa mazingira.

Kwa mujibu wa Mkonyi, mafanikio ya kazi hiyo yanapaswa kupimwa kwa athari zake kwa watu na jamii.

“Kwetu sisi Tanzania, mafanikio ya HRNS hatimaye yanaonekana katika maisha ya familia za wakulima wadogo, vijana na jamii tunazofanya nazo kazi,” alisema.

Aliongeza kuwa mabadiliko ya kudumu katika jamii za vijijini yanahitaji muda, ushirikiano na suluhisho zinazoendana na mazingira ya eneo husika.

Neumann, aliyeanzisha HRNS pamoja na familia yake mwaka 2005, amesimamia upanuzi wa taasisi hiyo kutoka mipango iliyolenga zaidi kahawa hadi kuwa taasisi pana ya maendeleo ya kimataifa.

Akieleza uamuzi wake wa kukabidhi nafasi hiyo, alisema:“Baada ya zaidi ya miaka 20, wakati umefika kwangu kukabidhi nafasi ya Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini kwa kizazi kijacho. Nafanya hivyo kwa kujiamini kwa sababu Hanns R. Neumann Stiftung ina msingi imara na iko tayari kuendelea kukua na kujiendeleza.”

Dkt. Smidt, ambaye ana uzoefu mkubwa katika ushirikiano wa kimataifa na maendeleo ya kimkakati ya mashirika yasiyo ya kiserikali, amesema uhusiano wake na HRNS umejengwa juu ya maadili yanayofanana na dhamira ya kuleta matokeo ya kudumu kupitia ushirikiano.

Kwa wakulima wa kahawa Tanzania, mafanikio ya uongozi mpya hatimaye yatapimwa si kwa mabadiliko yaliyofanyika katika uongozi wa taasisi, bali kwa matokeo yatakayoonekana katika vijiji vinavyolima kahawa—ikiwemo mashamba yenye uwezo mkubwa wa kustahimili changamoto, kuboreka kwa maisha ya kaya, kuimarika kwa mashirika ya wakulima, fursa zaidi kwa vijana na ulinzi bora wa maliasili.

Baada ya miaka 20 ya HRNS nchini Tanzania, mabadiliko haya yanafungua awamu mpya ya kuendeleza uzoefu, ushirikiano na rasilimali zilizojengwa, huku wakulima wakitarajia maboresho makubwa zaidi, yanayopimika na yenye kudumu katika maisha ya familia zinazotegemea kahawa.

Kuanzia Oktoba 1, 2026, Michael R. Neumann (Kulia) ataachia nafasi ya Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya HRNS baada ya zaidi ya miongo miwili, na nafasi hiyo kuchukuliwa na Dkt. Nina Smidt, (kushoto) mtendaji mwenye uzoefu wa kimataifa katika uendeshaji wa taasisi za kijamii, ambaye pia ni Mkurugenzi Mtendaji na Msemaji wa Bodi ya Siemens Stiftung.


GEITA: Kwa vijana walio nje ya mfumo rasmi wa elimu, kukosa ajira si lazima kuwe na maana ya kukosa kabisa fursa za kufanya kazi; wakati mwingine changamoto kubwa ni kukosa maarifa na ujuzi unaowawezesha kuzitambua na kuzitumia fursa zilizopo.

Hilo ndilo linalolenga kushughulikiwa na Mradi wa BRIDGE Tanzania, unaotekelezwa na Tume ya Taifa ya UNESCO ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Korea Kusini, kwa kuwapatia vijana walio nje ya mfumo rasmi wa elimu elimu ya msingi na ujuzi wa vitendo unaoweza kuwawezesha kujiajiri na kushiriki katika shughuli za kiuchumi.

Katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita, vijana 210 tayari wamepatiwa mafunzo kupitia mradi huo, huku baadhi yao wakianza kutumia ujuzi walioupata katika uzalishaji wa bidhaa mbalimbali, zikiwemo sabuni za miche, sabuni za maji na vyakula vya mifugo.


Mafunzo hayo pia yanahusisha kusoma, kuandika, kuhesabu na ujasiriamali, yakilenga kuwajengea vijana uwezo unaoweza kutumika katika maisha yao na katika mazingira ya soko.

Akizungumza wakati wa kikao cha Kamati ya Uongozi ya Wilaya (District Steering Committee) ya Mradi wa BRIDGE Tanzania kilichofanyika Nzera, Geita, Mratibu Msaidizi wa Kitaifa wa mradi huo, Adriano Adrian Hyera, alisema hadi sasa vijana 210 katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita wamepatiwa mafunzo.

Alisema mradi huo unaweka mkazo katika kuwapa vijana fursa ya kupata maarifa na ujuzi ambao unaweza kuwasaidia kujenga uwezo wa kujitegemea.


“Lengo si kuwapa vijana mafunzo pekee, bali kuwajengea uwezo ambao wataweza kuutumia baada ya mafunzo ili kujipatia kipato na kujitegemea,” alisema Hyera.

Kwa mujibu wa muundo wa mradi, vijana ambao hawakupata fursa ya kukamilisha elimu ya msingi hupewa nafasi ya kujenga uwezo katika kusoma, kuandika na kuhesabu, kabla ya kuendelea na mafunzo ya ujuzi wa vitendo unaoendana na mazingira yao na fursa zinazopatikana katika soko.

Mtazamo huo unaweka msisitizo katika kuunganisha elimu na ujuzi wa vitendo, ili kijana anapomaliza mafunzo asiishie kuwa na maarifa ya darasani pekee, bali awe na uwezo wa kutumia ujuzi huo katika shughuli za uzalishaji na kujiajiri.

Katika utekelezaji wake Geita, mradi unawawezesha vijana kujifunza kwa vitendo na pia unatoa vifaa na mahitaji muhimu kwa ajili ya mafunzo, ili kuwapa nafasi ya kufanya mazoezi ya uzalishaji wakati wa kujifunza.

Baadhi ya vijana walionufaika na programu hiyo wamesema mafunzo yamewajengea uwezo wa kufanya shughuli mbalimbali za uzalishaji na kuwapa mtazamo mpya kuhusu namna wanavyoweza kutumia ujuzi wao kama njia ya kujipatia kipato.

Ujuzi huo unawapa pia nafasi ya kutengeneza bidhaa ambazo zinaweza kutumika katika jamii na, kwa kuzingatia ubora na mahitaji ya soko, kuwa sehemu ya shughuli zao za kiuchumi.

Kutoka elimu ya msingi hadi ujuzi wa soko

Kwa mtazamo wa mradi, elimu na ujuzi haviwekwi katika maeneo mawili tofauti, bali vinaunganishwa ili kumjengea kijana uwezo wa kutumia maarifa yake katika mazingira halisi.

Baada ya kujenga msingi wa kusoma, kuandika na kuhesabu, kijana hupewa ujuzi wa vitendo unaozingatia eneo analotoka na fursa zinazopatikana katika soko.

Hii inalenga kuwapa vijana ambao hawakumaliza elimu rasmi nafasi ya kupata ujuzi unaoweza kuwasaidia kushindana katika shughuli za kiuchumi pamoja na vijana wengine waliopitia njia rasmi za elimu na mafunzo ya ufundi.

Kwa maana hiyo, BRIDGE Tanzania inalenga kujenga daraja kati ya elimu, ujuzi na soko, badala ya kuishia katika utoaji wa mafunzo pekee.

Vijana wahimizwa kutumia fursa za mikopo

Akizungumzia hatua zinazofuata baada ya mafunzo, Hyera aliwashauri vijana kujiunga katika vikundi vya watu watano ili waweze kuchangamkia fursa za mikopo zinazotolewa na Halmashauri.

Alisema ushiriki katika vikundi unaweza kuwasaidia vijana kutumia ujuzi walioupata katika shughuli za kiuchumi na kutafuta fursa za kukuza shughuli zao.

Hatua hiyo inalenga kuhakikisha kuwa mafunzo wanayopata vijana yanaunganishwa na fursa za mitaji na uzalishaji, ili kuongeza uwezekano wa ujuzi huo kuleta matokeo katika maisha yao.

Majaribio yenye matarajio ya kupanuka

BRIDGE Tanzania ni mpango wa majaribio unaotekelezwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita, Halmashauri ya Wilaya ya Masasi na Kaskazini A Unguja.

Mradi una lengo la kuwafikia vijana 3,000 katika kipindi cha miaka mitano, sawa na takribani vijana 600 kila mwaka.

Majaribio hayo yanatoa nafasi ya kutathmini namna ya kuwaunganisha vijana walio nje ya mfumo rasmi wa elimu na elimu ya msingi, ujuzi wa vitendo na fursa za kiuchumi.

Matokeo na uzoefu unaopatikana katika maeneo ya utekelezaji utasaidia katika kutathmini namna mfumo huo unavyoweza kuimarishwa na, baada ya tathmini, kupanuliwa katika maeneo mengine nchini.

Tume ya UNESCO katika utekelezaji

Utekelezaji wa BRIDGE Tanzania unaenda sambamba na juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita za kuwawezesha vijana kupata maarifa, ujuzi na fursa za kushiriki katika shughuli za kiuchumi na maendeleo ya Taifa.

Kupitia Tume ya Taifa ya UNESCO, ushirikiano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Korea Kusini umegeuzwa kuwa fursa ya kuwafikia vijana ambao kwa sababu mbalimbali hawapo katika mfumo rasmi wa elimu.

Tume ya Taifa ya UNESCO, kwa jukumu lake la kuratibu, kutathmini na kufuatilia utekelezaji wa shughuli za UNESCO nchini, inaendelea kushirikiana na Serikali na wadau mbalimbali katika kuhakikisha programu zinazotekelezwa zinachangia mahitaji na vipaumbele vya maendeleo ya Tanzania.

Kwa BRIDGE Tanzania, msisitizo ni kuhakikisha kijana aliye nje ya mfumo rasmi hapotezi fursa ya kujenga uwezo. Badala yake, anapewa nafasi ya kujifunza, kupata ujuzi na kuutumia katika kujenga maisha yake.

Kikao cha Kamati ya Uongozi ya Wilaya kilichofanyika Nzera, Geita, kilitoa nafasi kwa wadau kupitia utekelezaji wa mradi, mafanikio, changamoto na hatua zinazoweza kuchukuliwa ili kuongeza manufaa yake kwa vijana.

Kwa vijana hao 210 wa Geita, safari inaanzia katika kujenga msingi wa elimu na ujuzi; lakini lengo kubwa ni kuwawezesha kutumia uwezo huo katika ulimwengu halisi wa kazi, uzalishaji na kujitegemea.

▪️Waziri Mavunde na Waziri Kabamba wakubaliana msingi wa ushirikiano,

▪️Ni utekelezaji wa maelekezo ya Rais Samia na Rais Tshisekedi ya ushirikiano baina ya nchi hizo mbili,

▪️Ushirikiano walenga kurahisisha usafirishaji na biashara ya madini,

▪️Wakubaliana kuweka mikakati ya pamoja kuimarisha ufuatiliaji wa uzalishaji wa madini (traceability),


TIANJIN, CHINA

Pembezoni mwa Mkutano wa Madini wa China uliofanyika Jijini Tianjin, Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Madini wa Jamhuri ya Kidemokrasia  ya Kongo (DRC), Mheshimiwa Louis Watum Kabamba yaliyolenga kufungua ukurasa mpya wa ushirikiano kwenye sekta ya madini.

Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika tarehe 11 Septemba, 2026 Waziri Mavunde na mwenzake Mhe. Kabamba walijadiliana kwa kina namna ya kuendeleza sekta ya madini baina ya Nchi zao na hatimaye kuweka msingi ambao utakuwa ni mwanzo wa kuimarisha ushirikiano utakaoleta tija kwa pande zote mbili.

"Leo tumekutana hapa si kwa bahati mbaya, haya ni matokeo ya maelekezo ya viongozi wetu Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na Mhe. Felix Tshekedi ya kwamba Nchi zetu ni muda muafaka wa kuimarisha ushirikiano kwenye sekta ya madini kwani tunahitajiana na kutegemeana hususan katika masuala ya usafirishaji wa madini" 

"Viongozi wetu wameshatuwekea msingi, sisi kazi yetu ni kuhakikisha tunayaishi maono yao na kuimarisha ushirikiano ambao utakwenda kuongeza tija na kuboresha sekta zetu za madini kuanzia uzalishaji mpaka biashara na uongezaji thamani madini" alisisitiza Waziri Mavunde.

Aidha, Waziri Mavunde alibainisha kuwa ushirikiano baina ya Kongo DRC na Serikali ya Jamhuri ya Tanzania umelenga kwa kiasi kikubwa kurahisisha ufanyaji wa biashara na usafirishaji wa madini kwa maslahi mapana ya Nchi zetu.

Vilevile, Mavunde alieleza kuwa kwa sasa ni vyema Tanzania na DRC wakaweka mikakati ya pamoja na kuisimamia kwa lengo la kuimarisha ufuatiliaji wa mnyonyoro wa uzalishaji wa madini kuanzia yanapochimbwa mpaka yanapouzwa au kusafirishwa kwenda nje (traceability).

Naye, Waziri wa Madini wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo (DRC), Mhe. Louis Kabamba alishukuru kwa kukutana na mwenzake na kuahidi kuwa, kwa namna yeyote ni vyema kuyaishi maono ya Viongozi wakuu wa Mataifa haya ili kuleta manufaa yanayotarajiwa kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.

Aliendelea kusisitiza kuwa ushirikiano baina ya Tanzania na DRC pia utasaidia kubadilishana uzoefu wa namna ya kuendeleza sekta ya madini hususani katika kuwezesha uchimbaji mdogo na kuongeza mapato ya Serikali, hatua ambayo kwa DRC bado wachimbaji wadogo wanachangia kiasi kidogo. Pia, Mhe. Kabamba alisifu maendeleo ya STAMICO na kuomba uzoefu wao usaidie kuimarisha Shirika la Madini la Kongo ili liweze kuzalisha na kujiendesha kwa faida.








Kampeni ya Bonge la Wakala ya CRDB imechochea ushindani mkubwa miongoni mwa mawakala wa benki hiyo huku waliofanya vizuri zaidi katika kuongeza idadi ya miamala wakizawadiwa pikipiki 33 na mashine za POS 55  katika kipindi cha miezi mitano tangu kuanzishwa kwa kampeni hiyo.

Akizungumza mjini Morogoro wakati wa zoezi la kukabidhi zawadi hizo, Mkurugenzi wa Matawi wa CRDB Bank Tanzania, Bonaventura Paul Kiungo, amesema kampeni hiyo imechangia kuongeza mapato ya benki kwa asilimia 8, huku matumizi ya maeneo ya mawakala katika utoaji wa huduma kwa jamii yakifikia asilimia 90.

Amesema hali hiyo imesaidia kurahisisha upatikanaji wa huduma za kifedha na kutimiza mahitaji ya wateja katika maeneo mbalimbali nchini.

Katika zoezi hilo, jumla ya pikipiki 33 na mashine za POS 55 zilikabidhiwa kwa mawakala walioibuka washindi baada ya kufanya idadi kubwa ya miamala katika kipindi cha miezi mitano tangu kuanzishwa kwa kampeni ya Bonge la Wakala.

Kiungo amesema utoaji wa zawadi hizo ni sehemu ya malengo ya CRDB ya kuhamasisha mawakala kuongeza juhudi katika utoaji wa huduma na kupanua wigo wa huduma za benki kwa wananchi.

Ameongeza kuwa kampeni hiyo itaendelea kuwa endelevu, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa benki hiyo kukuza mtandao wa mawakala na kuhakikisha wateja wanapata huduma kwa urahisi zaidi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Mawakala wa CRDB, Abbas Abrahiman, amesema kampeni hiyo imeongeza chachu na ushindani miongoni mwa mawakala, hali ambayo imekuwa na mchango katika kuboresha utoaji wa huduma kwa wateja.

Naye Ester Raphael, mmoja wa mawakala walionufaika na zawadi hizo, amesema pikipiki waliyopewa itasaidia kuongeza ufanisi na ubora wa huduma kwa wateja, hasa katika kuwafikia wananchi kwa urahisi zaidi.

Kampeni ya Bonge la Wakala inalenga kuhamasisha mawakala kuongeza idadi ya miamala, kuboresha huduma na kuchochea matumizi ya huduma za kifedha kupitia mtandao wa mawakala wa CRDB nchini.









Top News