

ZAIDI ya watu 20 wanahojiwa na Jeshi la Polisi wilayani Same mkoani Kilimanjaro kwa tuhuma za kudaiwa kuendesha shughuli za uchimbaji haramu wa madini katika vyanzo vya maji ndani ya mita 60 kinyume cha sheria na kusababisha uharibifu mkubwa wa mazingira.
Akizungumza kuhusu hatua zinazochukuliwa jana ofisini kwake, Mkuu wa Wilaya ya Same, Kasilda Mgeni, alisema Kamati ya Usalama ya wilaya ilipata taarifa za siri kuhusu uchimbaji huo katika maeneo mbalimbali na kufika kujiridhisha, ambapo ilibaini kuwepo kwa shughuli hizo.
Alisema baada ya kubaini hali hiyo, Kamati iliunda timu ya kwanza ya wataalamu kutoka RUWASA, Bodi ya Maji Bonde la Pangani, Maafisa Mazingira na Maafisa Madini, iliyofanya uchunguzi katika maeneo yote na kubaini uchimbaji haramu katika kata saba pamoja na uharibifu mkubwa wa mazingira.
Kasilda alisema kuwa, iliundwa timu ya pili kutoka ndani ya Kamati ya Usalama kwa ajili ya kuwabaini wahusika waliotajwa katika taarifa za siri zilizotolewa na wananchi na baadhi ya madiwani wenye nia njema na wazalendo.
“Hadi sasa zaidi ya watu 20 wanaotuhumiwa kuhusika na uchimbaji huo pamoja na kupeleka mitambo wamehojiwa na Jeshi la Polisi, na wengine wanaendelea kuhojiwa kwa awamu ili kupata ushahidi na watakaobainika kuhusika watachukuliwa hatua za kisheria, na viongozi wa Serikali watakaobainika pia watachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria za utumishi wa umma,” alisema Kasilda.
Mkuu huyo wa Wilaya alisema hali kama hiyo iliwahi kutokea mwaka 2023, ambapo Kamati ya Usalama ilitembelea maeneo hayo na kufanikiwa kuwakamata zaidi ya watu watano waliokuwa wakijihusisha na uchimbaji haramu pamoja na mitambo yao, hali iliyofanya shughuli hizo kusitishwa kwa muda hata hivyo, alisema uchimbaji huo umeibuka tena mwaka huu na hatua za kuwadhibiti zinaendelea.
Pia, wachimbaji hao wamebainika kufanya shughuli za uchimbaji bila kuwa na vibali wala leseni kutoka kwenye mamlaka husika huku, Kasilda akiwaonya watu wanaopanga kurejea katika maeneo hayo na kuendelea na uchimbaji haramu, akisisitiza kuwa Serikali haitasita kuchukua hatua kali za kisheria dhidi ya watakaokiuka taratibu.
Kasilda alizitaka taasisi za Serikali zinazohusika na uhifadhi wa mazingira na ulinzi wa vyanzo vya maji kutekeleza majukumu yao ipasavyo kwa kufanya ukaguzi wa mara kwa mara na kuchukua hatua za kisheria.
Pia amewapongeza wananchi na baadhi ya madiwani waliotoa taarifa za siri na kusisitiza kuwa Serikali itawalinda.
Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro, SACP Saimon Maigwa alisema kuwa, Jeshi hilo limeshafungua jalada na kwa sasa linaendelea na uchunguzi ili kubaini ukweli wa jambo hilo.
Na Mwandishi wetu, Babati
Mkoa wa Manyara umeweka mkakati wa kuhakikisha watoto 670,000 wenye umri chini ya miaka 10 wanafikiwa na kupata chanjo katika Kampeni ya Chanjo ya Polio ya Matone, huku maandalizi ya Uzinduzi wa Kitaifa wa Kampeni hiyoyakiendelea kufanyika mkoani humo.
Akizungumza baada ya kupata nafasi ya kuonana na Kaimu Meneja Mpango wa Taifa wa Chanjo Dkt Georgina Joachim kutoka Wizara ya Afya pamoja na Dkt Floriani Tinuga kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI, Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Cuthbert Sendiga, amesema mkoa uko tayari kutekeleza zoezi hilo kwa ufanisi.
Mhe. Sendiga amesisitiza kuwa Serikali ya Mkoa imejipanga kuhakikisha hakuna mtoto atakayeachwa nyuma, na kwamba juhudi zote zitaelekezwa katika kuwafikia watoto wote 670,000 wanaolengwa kupata chanjo kuanzia tarehe 27 hadi 30 Agosti 2026.
Amesema ushirikiano kati ya Serikali, wataalamu wa afya, viongozi wa maeneo, wazazi, walezi na jamii kwa ujumla ni muhimu katika kuhakikisha kampeni hiyo inafikia malengo yaliyowekwa.
Kampeni hiyo inalenga kuimarisha kinga dhidi ya ugonjwa wa Polio kwa watoto na kuongeza uelewa wa jamii kuhusu umuhimu wa kuwapeleka watoto kupata chanjo kwa wakati.
Katika utekelezaji wa kampeni, timu za wataalamu wa afya zinatarajiwa kushirikiana na viongozi na jamii watapita nyumba kwa nyumba, mashuleni, kwenye minada, masoko, nyumba za Ibada na maendeo yenye mikusanyiko kuwatafuta na kuwapatia chajo walengwa wote wa zoezi hili.
Mkoa wa Manyara pia unaendelea na maandalizi kuelekea uzinduzi wa kampeni ya chanjo ya Polio ya Matone Kitaifa tarehe 27 Agosti 2026, huku uongozi wa Mkoa ukisisitiza utayari wake wa kuhakikisha zoezi hilo linafanyika kwa mafanikio.


Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imewataka Waandishi wa Habari wa Crown Media kulinda imani ya umma kwa kuzingatia weledi, maadili, uadilifu na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao.
Wito huo umetolewa wakati wa mafunzo ya siku mbili yaliyotolewa na JAB kwa Waandishi wa Habari wa Crown Media, kuanzia Agosti 18 hadi 19, 2026, jijini Dar es Salaam yakilenga kuwaongezea maarifa na kuwajengea uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria, maadili na viwango vya taaluma ya uandishi wa habari.
Akiwasilisha Mada kuhusu Msingi na Mfumo wa Kisheria unaosimamia Sekta ya Habari nchini Tanzania katika mafunzo hayo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, amewasihi Waandishi wa Habari kuthamini na kulinda taaluma yao kwa kuzingatia misingi inayowaongoza katika utekelezaji wa majukumu yao.

Kwa upande wake, Dkt. Egbert Mkoko amewataka Waandishi wa Habari kuzingatia maadili katika kila hatua ya kazi zao, akieleza kuwa maadili ndiyo msingi wa uandishi wa habari unaowajibika na wenye tija kwa jamii.
“Mwandishi wa Habari anapaswa kuzingatia maadili ya kazi katika kila hatua ya utekelezaji wa majukumu yake, kwa kuwa uadilifu na uwajibikaji ndiyo msingi wa taaluma hii,” amesema Dkt. Mkoko alipokuwa akifafanua mada Kuhusu Maadili ya Utangazaji na makosa ya kimaadili yanayofanywa mara kwa mara.
Naye Mjumbe wa JAB na Kaimu Meneja wa Huduma za Kiswahili wa Shirika la Magazeti ya Serikali (TSN), Bw. Mgaya Kingoba, akiwasilisha mada kuhusu uzalendo, amewataka Waandishi wa Habari kutumia taarifa kwa usahihi na kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia maslahi ya umma.

“Kwa kweli, changamoto tuliyonayo katika vyombo vyetu vya habari ni kushindwa kutofautisha maoni binafsi na uchambuzi wa kitaaluma, pamoja na kushindwa kutenganisha nafasi ya mtu binafsi na wajibu wake kama mwanataaluma. Pia kumekuwa na dhana kwamba Bodi ipo kwa ajili ya kuwadhibiti Waandishi wa Habari, pamoja na uelewa mdogo kuhusu ithibati, umuhimu wake na nafasi yake katika kulinda heshima ya taaluma,” amesema Imani Luvanga mmoja wa washiriki.
Mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa majukumu ya JAB kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, yanayolenga kuimarisha weledi, uadilifu, uwajibikaji na tija katika taaluma ya uandishi wa habari.






.jpeg)











.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)


.jpeg)


















.jpeg)
