Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, amewasili mkoani Arusha leo Jumatano, Septemba 16, 2026, ambapo amepokelewa katika Uwanja wa Ndege wa Arusha na Mkuu wa Mkoa wa Arusha, CPA Amos Makalla, pamoja na viongozi wengine wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Serikali.
Dkt. Mwigulu yupo mkoani Arusha kwa ajili ya shughuli mbalimbali za kikazi, ikiwemo kufungua rasmi Kongamano la Kitaifa la Wanamipango, litakalofanyika kesho Alhamisi, Septemba 17, 2026, katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano Arusha (AICC).
Afisa Mtendaji Mkuu wa Mixx Tanzania, Angelica Pesha (wa pili kulia), na Mratibu wa Jukwaa la Asasi za Kiraia Zanzibar (ZANGOF), Dkt. Mahfoudh Hassan Haji (katikati), wakionesha hati za makubaliano ya ushirikiano ambayo yatapanua upatikanaji wa huduma za kifedha za kidijitali kwa asasi za kiraia katika tukio lililofanyika leo visiwani humo.
Wanaoshuhudia ni Mrajisi wa Asasi za Kiraia Zanzibar, Ahmed Khalid Abdalla (wa pili kushoto), Mkuu wa Yas – Zanzibar, Mohamed Waqid (kulia) na Mwenyekiti wa ZANGOF Ndugu Hassan Hamis Juma (kushoto). Kupitia ushirikiano huo, wanachama wa ZANGOF wataweza kutumia Mixx Business Suite kufanya malipo na miamala mingine ya kifedha kidijitali.
WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali kupitia Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) itaanza kuchukua hatua za kuwasajili na kuwatambua watoto walio chini ya umri wa miaka 18, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha mfumo wa utambulisho wa Taifa.
Dkt. Mwigulu amesema hatua hiyo itamuwezesha kila Mtanzania kutambulika kuanzia hatua za mwanzo za maisha yake pamoja na kuondoa pengo lililokuwepo katika mfumo wa utambulisho kati ya mtoto anapozaliwa na anapofikisha umri wa miaka 18.
Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo, Jumatano, Septemba 16, 2026, wakati akiwa Mgeni Rasmi katika maadhimisho ya Siku ya Utambulisho Duniani, yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City, Dar es Salaam.
“Mfumo huu utasaidia kupunguza usumbufu wa kutumia nyaraka au vitambulisho vingi wakati wa kupata huduma mbalimbali, kwa kuwa taarifa muhimu za mwananchi zitaendelea kutambulika na kuhifadhiwa katika mfumo mkuu wa Taifa wa utambuzi” amesema.
Aidha, Dkt. Mwigulu amewataka Watanzania ambao tayari wamesajiliwa na vitambulisho vyao vya Taifa vimekamilika kwenda kuvichukua, akisisitiza kuwa utambulisho ni msingi muhimu wa maendeleo ya mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.
“Kitambulisho chenyewe kama nchi tumeingia gharama, tumeahirisha baadhi ya shughuli za maendeleo ili tutoe vitambulisho. Lakini tunapokuwa tumetoa kitambulisho, halafu mhusika haendi kuchukua, haya ni mambo ambayo yanakwamisha malengo mapana,” amesema.
Amesema kwa sasa NIDA imeboresha utaratibu wa kuwafahamisha wananchi pale vitambulisho vyao vinapokuwa tayari, ikiwemo kupitia ujumbe mfupi wa simu (SMS), hivyo hakuna sababu kwa wananchi waliokwishaandikishwa kuacha vitambulisho vyao kwa muda mrefu bila kuvichukua.
“Niendelee kusisitiza wananchi wote ambao wako tayari na vitambulisho vyao, basi waende kuvichukua. Lengo letu ni kuona kuwa hakuna Mtanzania anayeachwa nyuma katika kupata vitambulisho vya Taifa,” amesema.
Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu amesema Serikali imeendelea kufanya maboresho katika mfumo wa utambulisho wa Taifa ili kuhakikisha unakidhi mahitaji ya sasa ya kiteknolojia, usalama wa taarifa na utoaji wa huduma kwa wananchi.
“Serikali imeendelea kuboresha mfumo wa utambulisho ili kupunguza utegemezi wa vitambulisho vingi kwa huduma mbalimbali na kuelekea katika mfumo ambao taarifa muhimu za mwananchi zinapatikana kupitia mfumo mkuu wa Taifa wa utambuzi,” amesema.
Naye, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Patrobas Katambi, amesema NIDA imefanya mapitio ya jumla ya vitambulisho vilivyotolewa katika ofisi zake na vituo 10 vya usajili vilivyopo katika kila wilaya, bila kuhusisha vituo 156 vilivyotajwa awali.
Amesema hadi sasa jumla ya watu 27,520,835 wamesajiliwa, ambapo watu 23,515,667 wamekwishapatiwa Namba za Utambulisho wa Taifa. Aidha, vitambulisho 21,526,635 vimezalishwa, huku bado kukiwa na idadi ya vitambulisho ambavyo havijachukuliwa na wananchi waliostahili kuvipata.
Kwa Upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa NIDA, James Kaji, amesema jamii inapaswa kuacha dhana kwamba NIDA ni taasisi inayotoa kadi pekee, kwa kuwa utambulisho wa Taifa ni msingi wa upatikanaji wa huduma na utambulisho wa mwananchi katika maisha yake yote.
Amesema NIDA inaendelea kuboresha kitambulisho cha Taifa ili kiwe cha kidijitali na kiweze kuhusisha taarifa muhimu za huduma mbalimbali za kijamii, ikiwemo cheti cha kuzaliwa, bima ya afya, TIN, leseni ya udereva na taarifa nyingine muhimu, huku taarifa za kiafya kama kundi la damu zikitarajiwa kusaidia wakati wa dharura, kwa kuzingatia uthibitisho wa kitabibu.
Kanji amesema usajili wa watoto tangu wanapozaliwa ni muhimu kwa sababu utamwezesha kila mtoto kutambulika na kupata huduma za kijamii kwa urahisi katika hatua zote za maisha. Amesema zoezi hilo litaanza kwa majaribio katika wilaya za Kilolo, Lungu na Kusini Unguja, kabla ya kupanuliwa katika maeneo mengine nchini.
Katika mkutano wake na Mkurugenzi Mkuu wa IAEA, Bw. Rafael Mariano Grossi, mazungumzo yalijikita katika kuimarisha ushirikiano katika matumizi ya sayansi na teknolojia ya nyuklia kwa madhumuni ya amani na maendeleo, hususan matibabu ya saratani, kilimo na usalama wa chakula, lishe, maendeleo ya wataalamu pamoja na maandalizi ya Tanzania kuelekea matumizi ya nishati ya nyuklia kama nyongeza ya vyanzo vya uzalishaji umeme nchini siku zijazo.
Aidha, Makamu wa Rais amefanya mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa Vienna (UNOV) na Mkurugenzi Mtendaji wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Dawa za Kulevya na Uhalifu (UNODC), Dkt. Monica Juma. Mazungumzo yaliyolenga kuendeleza ushirikiano baina ya Tanzania na UNODC katika juhudi za kudhibiti dawa za kulevya.
Makamu wa Rais, Mhe. Ndejembi, yuko Jijini Vienna, Austria, akimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Mkutano Mkuu wa 70 wa Wakala wa Kimataifa wa Nguvu za Atomu (IAEA), unaowakutanisha Viongozi na Wawakilishi wa Nchi wanachama kujadili masuala mbalimbali yanayohusu matumizi salama na ya amani ya sayansi na teknolojia ya nyuklia.
TANZANIA kupitia Benki Kuu (BoT) imepata tuzo tano za utambuzi zilitolewa na Jumuiya ya Huduma Jumuishi za Fedha( AFI) ikiwa ni sehemu ya kutambua hatua mbalimbali ilizochukua katika kuimarisha huduma jumuishi za kifedha.
Akizungumza leo Septemba 16,2026 jijini Dar es Salaam mbele ya waandishi wa habari kuhusu tuzo hizo Meneja wa Huduma Jumuishi za Kifedha wa Benki Kuu ya Tanzania, Nangi Massawe amesema AFI ilianzishwa mwaka 2009 .
Ameongeza kuwa AFI ina wanachama kutoka nchi 84 wakati taasisi wanachama zikifikia 90 huku lengo ni kuhakikisha wananchi wanapata na kutumia huduma rasmi za kifedha kwa usalama na kwa manufaa ya maendeleo yao na uchumi wa nchi.
Ameongeza mkutano wa AFI uliofanyika Septemba mosi hadi 4, mwaka huu nchini Guinea, Tanzania kupitia Benki Kuu imepata tuzo tatu kwa upande wa taasisi na tuzo mbili watu binafsi kutokana na utekelezaji wa mikakati ya huduma jumuishi za kifedha.
Amesema tuzo ya kwanza ni Maya Declaration Award, iliyotolewa kutokana na utekelezaji wa ahadi zilizowekwa na Tanzania, ambapo kati ya ahadi 13, nchi imetekeleza sita ikiwemo kuandaa na kutekeleza mkakati wa Huduma Jumuishi za Kifedha.
“Kwa sasa Tanzania inatekeleza mkakati wa tatu wa huduma jumuishi za kifedha uliowekwa mwaka 2023 na utatekelezwa kwa kipindi cha miaka mitano hadi mwaka 2028,” amesema Nangi
Pia amesema mafanikio mengine yaliyotambuliwa ni kuongezeka kwa kiwango cha ujumuishi wa kifedha kutoka asilimia 65 mwaka 2017 hadi asilimia 76 mwaka 2023, huku vipimo vya ndani vikionyesha kiwango hicho kimeendelea kukua na kufikia asilimia 80.
Nangi amesema idadi ya watu wazima wasio na huduma za kifedha nayo imepungua kutoka milioni 7.8 mwaka 2017 hadi milioni 6.4 mwaka 2022, wakati upatikanaji wa huduma za kifedha ndani ya umbali wa kilomita tano umeongezeka kutoka asilimia 86 hadi 89.
Pia amesema matumizi ya huduma za fedha kwa njia ya simu yameongezeka kutoka asilimia 60 hadi asilimia 72, huku pengo la huduma za kifedha kati ya wanawake na wanaume likipungua kutoka asilimia 10 mwaka 2017 hadi asilimia 3.2 mwaka 2022.
“Tanzania pia imeweka mfumo maalumu wa kumlinda mtumiaji wa huduma za kifedha kwa kuhakikisha malalamiko yanafikishwa sehemu sahihi na kufanyiwa kazi, pamoja na kuanzisha programu za elimu ya fedha kwa walio ndani na nje ya mfumo wa shule,”amesema Nangi.
Aidha amesema tuzo nyingine ilitokana na mafanikio ya sera za ujumuishi wa kifedha zinazozingatia wanawake, ikiwemo kuweka kipengele maalumu cha jinsia katika mkakati wa sasa, kubuni bidhaa zinazokidhi mahitaji ya wanawake, kupunguza vikwazo vya upatikanaji wa huduma na kuwezesha wanawake kupata huduma za mikopo na huduma nyingine rasmi za kifedha.
Kuhusu tuzo mbili za mtu binafsi amesema zikitolewa kwa watumishi wa Benki Kuu, akiwemo Dk. Khadija Kishimba na Nangi Massawe kwa kutambuliwa katika maeneo ya uongozi wa kiufundi na sera za huduma jumuishi za kifedha.
Awali Meneja Mifumo ya Malipo ya Taifa kutoka BoT, Mutashobye Mushumbusi ameeleza kuwa benki hiyo imeweka mwongozo wa gharama za huduma za kifedha kwa lengo la kuhakikisha wananchi wanapata huduma hizo kwa gharama nafuu.
“Mwongozo huo umeandaliwa kwa kushirikisha watoa huduma za kifedha na tayari umeanza kutumika,unasaidia kupunguza gharama za baadhi ya huduma,”amesema na kusisitiza BoT imeweka mkakati wa kuhakikisha taarifa za gharama za huduma za kifedha zinawekwa wazi kupitia tovuti pamoja na kuwataka watoa huduma kuonesha gharama hizo katika maeneo wanapotoa huduma.
Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira Tanzania (TRAMEPRO) limetoa salamu za pongezi kwa Baba Mtakatifu Leo XIV, katika kuadhimisha siku yake ya kuzaliwa, likimtakia afya njema, hekima, nguvu na neema katika kuendelea kutekeleza majukumu yake ya kichungaji.Katika salamu hizo, TRAMEPRO limemshukuru Mwenyezi Mungu kwa zawadi ya maisha ya Baba Mtakatifu, huku likitambua uongozi wake wa hekima, unyenyekevu na dhamira ya kulitumikia Kanisa.
Shirika hilo pia limeeleza kuthamini ujumbe wa Baba Mtakatifu unaohimiza amani, umoja, huruma, heshima ya utu wa mwanadamu na mshikamano, sambamba na wito wa kulinda mazingira na dunia ambayo imekabidhiwa kwa binadamu.
TRAMEPRO limesema ujumbe huo una umuhimu katika kipindi ambacho dunia inakabiliwa na changamoto mbalimbali, ikiwemo mabadiliko ya tabianchi, uharibifu wa mazingira, umasikini na changamoto za afya.
Kwa mujibu wa shirika hilo, afya ya mwanadamu haiwezi kutenganishwa na afya ya mazingira, kwa kuwa maji safi, udongo salama, hewa safi, mimea ya dawa na mazingira bora ni sehemu muhimu ya maisha na ustawi wa jamii.
TRAMEPRO limemtakia Baba Mtakatifu Leo XIV maisha marefu yenye afya njema na utume wenye mafanikio, huku likimuombea aendelee kuwa sauti ya matumaini, amani na upendo kwa watu wote, wanyonge, wagonjwa na wanaohitaji faraja.
Katika salamu hizo, TRAMEPRO limesisitiza kuwa:
“Afya ya mwanadamu na afya ya mazingira ni urithi wa pamoja unaopaswa kulindwa kwa kizazi cha sasa na vizazi vijavyo.”
Salamu hizo zimetolewa na Boniventura F. Mwalongo, Katibu Mkuu wa Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira Tanzania (TRAMEPRO).
TRAMEPRO limemalizia kwa kumtakia Baba Mtakatifu Leo XIV baraka na ulinzi wa Mungu, huku likiombea Kanisa, Tanzania, Afrika na dunia kwa ujumla.
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Charles Makongoro amewaomba wananchi na wadau mbalimbali kushiriki kikamilifu katika maandalizi ya kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2026, kinachotarajiwa kufanyika mkoani humo
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Makongoro amesema kilele hicho kitafanyika Jumatano, Oktoba 14, 2026, katika viwanja vya Nelson Mandela, Manispaa ya Sumbawanga.
Amesema shughuli za kilele hicho zitaambatana na matukio mbalimbali, ikiwemo maonesho ya fursa na shughuli za vijana, yatakayofanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi Ndua kuanzia Oktoba 8 hadi Oktoba 14, 2026.
Aidha amesema kutakuwa na Misa ya Kumbukizi ya miaka 27 ya kifo cha Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere itakayofanyika katika Kanisa Kuu Jimbo Katoliki Sumbawanga saa 12:00 asubuhi ya Oktoba 14, 2026, kabla ya kuendelea na sherehe za kilele cha Mwenge katika viwanja vya Nelson Mandela.
Aidha amewataka wananchi wa Rukwa kutumia fursa hiyo kujiinua kiuchumi kwa kufanya biashara mbalimbali, zikiwemo huduma za chakula, malazi, usafiri na usafirishaji kwa wageni watakaofika mkoani humo.
Amesema mkoa umejipanga kuhakikisha maandalizi ya kilele hicho yanafanyika kwa kushirikiana na Halmashauri zote nne,taasisi za umma, wadau na wananchi, huku akitoa wito kwa wananchi kushiriki katika kulinda amani na usalama wakati wa shughuli hizo .
Aidha Makongoro amesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa wananchi na wadau mbalimbali katika kuhakikisha kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2026 kinafanyika kwa mafanikio huku akiwataka wananchi kutumia tukio hilo kama fursa ya kukuza shughuli zao za kiuchumi na kudumisha amani na usalama wakati wote wa shughuli hizo.
Kilele hicho ni tukio muhimu la kihistoria kwa mkoa huo kuwa ni mara ya kwanza baada ya miaka 24 kwa mkoa huo kuwa mwenyeji wa kilele cha mbio za mwenge wa uhuru kitaifa ambapo uliwahi kuwashwa mkoani humo mwaka 1983 na 2002.
Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB), ipo mbioni kuzindua mwongozo wa tathmini ya misingi ya utawala nchini.
Mwongozo huo umelenga kuangalia hali ya uzingatiwaji wa misingi ya utawala bora na kuweka mfumo unaoweza kutumika kupima namna taasisi za umma, binafsi na mifumo ya utawala inavyotekeleza misingi ya utawala bora.
Mwongozo huo pia imelenga kuwa nyenzo muhimu katika kubaini mafanikio yaliyofikiwa, changamoto zilizopo na maeneo yanayohitaji maboresho katika nyanja ya utawala bora.
Akizungumza katika kikao kazi cha kupitia rasimu hiyo kilichofanyika katika ukumbi wa Mkuu wa Mkoa Jijini Dodoma leo, Kaimu Katibu Mtendaji wa THBUB, Bi. Suzan Ndeona amesema kazi ya uandaaji wa nyaraka hiyo muhimu kwa nchi, ilianza rasmi mwaka 2023 kwa kuangalia vigezo mbalimbali na uhitaji wa nchi wa kuwepo mwongozo na nyenzo itakayotumika katika kufanya tathmini ya Utawala Bora nchini.
Bi. Suzan amesema mwongozo huo umeweka vigezo vyote muhimu vya upimaji wa uwepo wa utawala bora katika Taasisi. Aidha ameeleza mwongozo huo utaendelea kuboreshwa ili kuhakikisha unaenda sambamba na mabadiliko mbalimbali ya kimfumo yanayoendelea nchini kama vile upimaji wa Watumishi wa Umma (PEPMIS).
“Bado mwongozo huu ni rasimu, utakapokamilika utawekwa mezani kupata maoni ya taasisi za umma, binafsi, na mashirika mbalimbali ambayo yanahusika na masuala ya utawala bora”. Amesema Bi. Suzan.
Miongoni mwa misingi muhimu itakayoangaliwa na kufanyiwa tathimini ni pamoja na uwazi, uwajibikaji, usawa, utawala wa sheria, ushirikishwaji, ufanisi na tija, maridhiano, mwitikio na uadilifu.
Akieleza kuhusu misingi ya utawala bora, Bi. Suzan alisema misingi hiyo ina uhusiano wa moja kwa moja na jamii kwa kuwa utawala bora huonekana kupitia taasisi zinavyotoa huduma, kusikiliza wananchi, kutumia rasilimali na kutekeleza majukumu kwa mujibu wa sheria.
Naye Bi Hellen Siriwa kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) wakati wa kutoa wasilisho la rasimu hiyo, amesema NBS imeshirikiana kikamilifu na THBUB katika kuandaa nyenzo za kufanyia tathmini kwa kuangalia namna ambavyo nchi itafaidika na mwongozo huo ulioandaliwa. Aliongeza kuwa NBS itaendelea kushirikiana na THBUB katika kuhakikisha kuwa mwongozo huo unakamilika na kuweza kuzinduliwa rasmi Kitaifa.
Mwongozo huo utakuwa nyenzo ya kujenga utamaduni wa uwajibikaji katika taasisi za umma na binafsi kwa kutambua mapema maeneo yenye changamoto na kuchukua hatua za maboresho kabla ya kutokea kwa madhara.
Mgalu amesema hayo Jumatatu Septemba 14, 2026 Jijini Mwanza wakati akifungua Mkutano wa Mwaka wa Wajiolojia Tanzania ambapo alishiriki kama mgeni rasmi katika tukio hilo akiambatana na baadhi ya wajumbe wa kamati hiyo.
Katika hotuba yake ya ufunguzi, Mgalu amesema kuwa kukosekana kwa bodi ya kusimamia weledi wa kada ya wanajiosayansi kumesababisha uwepo wa vishoka wanaofanya kazi za kijiolojia bila ya kuwa na sifa stahiki hivyo kusababisha hasara kwa wawekezaji na Serikali kwa ujumla.
“Jambo hili limesababisha kutokukuwepo kwa mfumo thabiti wa kudhibiti maadili, viwango, taaluma, weledi na utaalamu wa wanajiosayansi walio katika utumishi wa umma na katika sekta binafsi nchini”
Kwa upande wao, Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini walioshiriki Mkutano wa Wajiolojia kwa mwaka 2026 akiwemo Mbunge wa Geita Vijijini, Joseph Musukuma na Mbunge wa Jimbo la Katoro, Kija Ntemi wamesema suala la uanzishwaji wa Bodi ni la msingi watahakikisha wanaibeba ajenda hii kikamilifu.
Wadau mbalimbali wa sekta ya Uchukuzi na Usafirishaji wamekutana mjini Kigoma katika kikao cha siku moja kilichoandaliwa na Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), kwa lengo la kujadili fursa na changamoto zinazohusiana na usafirishaji wa mizigo na namna ya kuimarisha biashara katika ukanda wa Magharibi na Maziwa Makuu.
Kikao hicho kimehudhuriwa na wadau mbalimbali kutoka katika sekta ya Uchukuzi na Usafirishaji, ambapo Mgeni Rasmi, Mkuu wa Wilaya ya Kigoma, Dkt. Rashid Chuachua, kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, amesisitiza umuhimu wa ushirikiano miongoni mwa wadau katika kuimarisha ufanisi wa usafirishaji na kukuza biashara ya kikanda.
Kwa upande wa TPA, Naibu Mkurugenzi Mkuu, Mha. Dkt. Baraka Mdima, ameshiriki kikao hicho kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TPA, akiwakilisha uongozi wa Mamlaka katika majadiliano yaliyolenga kubaini maeneo ya kimkakati ya kuboresha huduma na kuongeza ufanisi wa usafirishaji kupitia Bandari ya Kigoma.
Majadiliano katika kikao hicho yamejikita katika kubaini changamoto zinazokwamisha mtiririko wa mizigo, zikiwemo vikwazo visivyo vya kiforodha, ucheleweshaji na gharama za usafirishaji, pamoja na kutafuta suluhu za pamoja zitakazoboresha mazingira ya biashara na kuongeza ushindani wa njia za usafirishaji.
Aidha, wadau wamejadili umuhimu wa kuimarisha matumizi ya Bandari ya Kigoma kama lango muhimu la biashara katika ukanda wa Maziwa Makuu, hususan kupitia Ushoroba wa Kati (Central Corridor) unaoiunganisha Tanzania na nchi jirani.
Kikao hicho pia kimekuwa fursa ya kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali, sekta binafsi na wadau wengine wa mnyororo wa usafirishaji katika kuboresha huduma, kupunguza muda na gharama za usafirishaji, na kuweka mazingira rafiki zaidi kwa biashara ya ndani na ya kikanda.
Kwa ujumla, kikao hicho kimeendelea kuonesha umuhimu wa majadiliano ya pamoja katika kutatua changamoto za usafirishaji na kutumia fursa zilizopo katika ukanda wa Magharibi, huku Bandari ya Kigoma ikiendelea kuwa sehemu muhimu ya kuunganisha biashara ya Tanzania na masoko ya nchi za Maziwa Makuu.
Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) wilaya ya Chamwino imefungua barabara ya Manda–Mafurungu yenye urefu wa kilomita 25 hatua ambayo imebadili hali ya usafiri na usafirishaji kwa wananchi wa kijiji cha Mafurungu baada ya kukabiliwa na changamoto ya muda mrefu ya kutokuwa na barabara.
Akizungumza kuhusu maendeleo ya mradi huo, Meneja wa TARURA wilaya ya Chamwino Mhandisi Richard Sanga amesema, barabara hiyo imefunguliwa ikiwa ni jitihada za serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuunganisha wananchi na kurahisisha shughuli za kiuchumi na kijamii.
Amesema TARURA wilaya ya Chamwino inahudumia mtandao wa barabara wenye urefu wa kilomita 1,297 huku ujenzi wa barabara ya Manda–Mafurungu ukiwa ni muhimu kwa wananchi wa vijiji vya Manda na Mafurungu kwa ajili ya kurahisisha upatikanaji wa huduma za afya na elimu, kupunguza gharama za usafiri na kufungua fursa za kiuchumi.
"Awali barabara hii haikuwepo kabisa lakini baada ya kupata fedha tumeweza kuifungua, mkandarasi tayari ameshafungua kilomita zote 25 huku kazi zinazoendelea ni ujenzi wa makalavati, uwekaji wa kifusi katika maeneo korofi na maandalizi ya uchongaji wa mifereji kwa ajili ya kudhibiti na kuondoa maji ya mvua barabarani", amesema.
Ameeleza kuwa kutokana na umuhimu wa barabara hiyo katika bajeti ya mwaka huu wa fedha wataweka changarawe katika baadhi ya maeneo korofi huku mpango wa mwaka ujao wa fedha ukiwa ni kuweka kifusi barabara yote na kumalizia makalavati ili kuhakikisha barabara inapitika kwa urahisi na kwa uhakika kipindi chote cha mwaka.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa kitongoji cha Machimbo, Bw. Mrisho Ally amesema kabla ya barabara hiyo wananchi wa Mafurungu wakitaka kusafiri hadi Dodoma mjini safari ya kwenda na kurudi walikuwa wakitumia nauli zaidi ya Sh. 100,000/= hali iliyowalazimu kutumia muda mwingi na gharama kubwa.
Amesema kwa sasa gharama hiyo imeshuka hadi Sh. 24,000/= kwa safari ya kwenda na kurudi huku magari yakiwa yanafika moja kwa moja kijijini ambapo imepunguza gharama na muda wa usafiri.
Ameongeza kuwa eneo hilo lina shughuli kubwa za uchimbaji wa madini ya dhahabu zinazochangia uchumi wa wilaya ya Chamwino hivyo ameiomba serikali kuendelea kuboresha barabara hiyo ili iweze kutoa huduma kwa wananchi na wafanyabiashara katika kipindi cha mwaka mzima.
Naye, Bw. Zabroni Matonya mkazi wa Mafurungu na mwekezaji katika shughuli za uchimbaji madini amesema, barabara hiyo imekuwa mkombozi kwa wachimbaji na wawekezaji kutokana na kurahisisha usafirishaji wa vifaa na malighafi kwani awali ubovu wa barabara uliwafanya kutumia muda mrefu kusafirisha malighafi zao mjini hivyo ameishukuru serikali kwa barabara hiyo.
Mkazi wa Mafurungu Bi. Salma Mtacha amesema kabla ya barabara wanafunzi walikuwa wakitembea umbali mrefu kufika shuleni hali iliyokuwa ikiwatia hofu wazazi lakini sasa barabara imefunguka wanafunzi wanafika shuleni bila shida pia wananchi wanafika katika vituo vya afya na hospitali bila changamoto jambo ambalo limeongeza usalama na ustawi wa jamii.
Naye, Selemani Bundala mkazi wa Mafurungu amesema awali safari ya kutoka kijijini hadi Dodoma mjini kwa pikipiki ilikuwa ikigharimu hadi Sh. 100,000/= lakini baada ya barabara kufunguliwa hali imebadilika na mabasi sasa yanafika moja kwa moja kijijini.
Amesema wananchi wanathamini jitihada za serikali katika kufungua barabara hiyo na ameomba kazi ya uboreshaji iendelee hadi barabara hiyo iweze kupitika mwaka mzima.







.jpeg)

.jpeg)


.jpeg)






.jpeg)







.jpeg)
.jpeg)




.jpeg)














.jpeg)

