Na Mwandishi Wetu, Morogoro Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA) umeeleza kuwa Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja umeendelea kuhakikisha Tanzania inapata bidhaa za mafuta kwa uhakika, kwa wakati na kwa gharama shindani.
Akizungumza katika Maonesho ya Nne ya Kitaifa ya Utamaduni yanayoendelea mkoani Morogoro, Mchumi wa PBPA, Bw. Henry Kilenga, amesema mfumo huo unahusisha ukusanyaji wa mahitaji ya mafuta kutoka kwa kampuni za uuzaji wa mafuta nchini kabla ya kutangazwa kwa zabuni za kimataifa.
Amesema PBPA hukusanya mahitaji hayo na kuyaunganisha ili mafuta yaagizwe kwa pamoja kwa kiwango kikubwa. Utaratibu huo huiwezesha nchi kunufaika na ununuzi wa pamoja na kupata gharama shindani za uagizaji na usafirishaji.
“PBPA hukusanya mahitaji ya mafuta kutoka kwa kampuni za uuzaji wa mafuta, huandaa zabuni na kuwashindanisha wazabuni waliokidhi vigezo. Utaratibu huu unasaidia kuhakikisha nchi inapata mafuta kwa uhakika na kwa gharama shindani,” amesema Kilenga.
Amefafanua kuwa zabuni hizo hushirikisha kampuni za kimataifa zilizohakikiwa na kukidhi vigezo vilivyowekwa na PBPA. Wazabuni hushindanishwa kwa uwazi, huku tathmini ikizingatia bei zilizowasilishwa, uwezo wa kusambaza mafuta na masharti mengine ya zabuni.
Kwa mujibu wa Kilenga, baada ya kukamilika kwa tathmini, kampuni zilizokidhi vigezo na kuwasilisha bei nzuri huchaguliwa kuleta mafuta nchini kulingana na kiasi na muda uliopangwa.
Kilenga amesema uwazi na ushindani katika uendeshaji wa zabuni unalenga kulinda maslahi ya taifa, kuongeza ufanisi na kuhakikisha bidhaa za mafuta zinaendelea kupatikana kwa ajili ya wananchi na shughuli mbalimbali za kiuchumi.
Amesisitiza kuwa Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja una mchango mkubwa katika kuimarisha usalama wa upatikanaji wa nishati na kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.

Zaidi ya wakulima 2000 mkoani Mwanza wanatarajiwa kunufaika na kilimo cha umwagiliaji mwaka mzima baada ya Serikali kuwagawia pampu za kisasa 164.
Wakulima hao ambao asilimia 70 ni vijana, wanatoka katika vikundi 125 vinavyotoka kwenye wilaya sita za mkoa wa Mwanza.
Akikabidhi pampu hizo leo Alhamisi kwa niaba ya aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Said Mtanda, Mkuu wa Wilaya ya Magu, Jubilate Lawuo amesema pampu hizo zitaongeza kasi ya uzalishaji wa mazao mbalimbali kwa wakulima na kuchangia katika mapinduzi ya kilimo mkoani humo.
Amesisitiza kuwa ugawaji wa pampu hizo unapaswa kuenda sambamba na utoaji elimu kwa wakulima kutoka kwa maofisa ugani waliosambazwa katika kata na vijiji mkoani humo.
Aidha, amewaasa wakulima kutumia pampu hizo kwa lengo lililokusudiwa ili kuleta matokeo chanya katika shughuli zao za kilimo.
Kwa upande wake Mwakilishi kutoka Tume ya Umwagiliaji mkoa wa Mwanza, Mhandisi Said Kambi amesema pampu hizo zilizogharimu jumla ya shilingi bilioni 1.1 zitagawanywa kwa vikundi 125 vya wakulima.
“Mkoa wa Mwanza una hekta 40,000 zinazofaa kwa kilimo cha umwagiliaji lakini ni hekta 3,300 zimeendelezwa kwa ajili ya kilimo hicho. Hivyo ujio wa pampu hizi utasaidia kuongeza kasi ya uzalishaji wa mazao katika kipindi chote cha mwaka.
“Ili kulinda mazingira na kuzuia kilimo cha pembezoni mwa vyanzo vya maji, zimefungwa mipira yenye urefu wa zaidi ya mita 60 kutoka kwenye vyanzo vya maji, mifereji au mabwawa,” amesema.
Kila pampu ina uwezo wa kusukuma mita za ujazo 80 hadi 100 za maji kwa saa, hatua inayoiwezesha kumwagilia hadi ekari 40 kwa siku, huku uwepo wa magurudumu ukiwezesha urahisi wa kuzihamisha.
Naye Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Magu, Edward Kihamba mbali na kuishukuru serikali kwa kuwapatia pampu 47 katika wilaya hiyo, pia ameahidi kushirikiana na madiwani wenzake kuhakikisha maofisa ugani wanatoa elimu inayotakiwa katika matumizi ya pampu hizo.
NMB, BUNGE KUWAKUTANISHA ZAIDI YA 1,000 MICHEZONI DODOMA
Na Mwandishi Wetu, Dodoma.
ZAIDI ya washiriki 1,000 kutoka Bunge, wizara 14 na taasisi 10 wanatarajiwa kushiriki NMB Bunge Bonanza 2026 litakalofanyika Jumamosi jijini Dodoma, baada ya NMB Bank Plc kukabidhi udhamini wake wathamani ya Sh milioni 210 ikiwemo vifaa vya michezo kwa ajili ya mashindano hayo.
Mwenyekiti wa Bunge Bonanza na Mbunge wa Makete, Festo Sanga, amesema mwaka huu Spika wa Bunge, Mussa Azzan Zungu, amealika wizara 14 na taasisi nyingine 10. Idadi ya washiriki inatarajiwa kuwa kubwa kuliko miaka iliyopita, huku akiongezea bonanza hilo litafanyika katika viwanja vya Shule ya Sekondari John Merlini, jijini Dodoma, Jumamosi, Agosti 29, 2026.
Mshauri Mwandamizi wa Kitengo cha Biashara za Serikali Benki ya NMB, Vicky Bishubo, amesema benki inaunga mkono michezo kwa sababu ya mchango wake katika afya, mshikamano na tija kazini. Vifaa vilivyokabidhiwa ni pamoja na mipira, makombe, track suti za michezo, fulana na medali.
Spika Zungu anatarajiwa kuwa mgeni rasmi. Kabla ya bonanza kuanza, wabunge watafanya matembezi yatakayoanzia Chuo cha Mipango saa 12:00 asubuhi.
Ingawa ushindani mkali unatarajiwa kutoka kwa timu za Bunge, wizara, taasisi na NMB, Sanga alisema lengo kuu ni kuwavuta watumishi kwenye mazoezi, kujenga mshikamano na kuongeza uelewa kuhusu kinga dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza.
BUNGE la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania leo (Ijumaa, Agosti 28, 2026) limemthibitisha Mheshimiwa Deogratius Ndejembi kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mheshimiwa Ndejembi amepitishwa kwa asilimia 100 ya kura zote 324 zilizopigwa na waheshimiwa wabunge, ambapo amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa imani aliyoionesha kwake kwa kumteua kuwa Makamu wa Rais na katika nafasi nyingine mbalimbali za uongozi.
Pia Mheshimiwa Ndejembi amelishukuru Bunge kwa imani kubwa waliyompa kiasi cha kumpigia kura kwa asilimia mia moja.
Mapema akiwasilisha hoja ya kuthibitisha uteuzi wa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Mheshimiwa Deogratius Ndejembi anatosha na ni mtu sahihi wa kumsaidia Mheshimiwa Rais katika nafasi ya Makamu wa Rais,
akiitaja kuwa ni nafasi yenye dhamana na majukumu makubwa katika uongozi wa nchi.
"Majukumu hayo yanahitaji mtu mwenye uzoefu wa uongozi, uelewa mpana wa shughuli za Serikali, uwezo wa kufanya kazi kwa karibu na Rais, busara katika kushughulikia masuala ya kitaifa, pamoja na uwezo wa kuratibu na kufuatilia utekelezaji wa majukumu mbalimbali ya Serikali," amesema Dkt. Mwigulu.
"Mheshimiwa Rais amemteua Mheshimiwa Deogratius John Pancras Ndejembi kwa kuzingatia, pamoja na mambo mengine, uzoefu alioujenga katika uongozi wa kisiasa na katika nafasi mbalimbali za Serikali," ameongeza Waziri Mkuu.
Dkt. Mwigulu amesisitiza kuwa uzoefu wa uongozi alionao Mheshimiwa Deogratius Ndejembi unadhihirisha kuwa ni mtu sahihi kutumikia wadhifa wa Makamu wa Rais.
"Mheshimiwa Deogratius John Pancras Ndejembi si mgeni katika uongozi wa Umma na katika siasa za nchi yetu. Kabla ya kuwa Mbunge, Mheshimiwa Ndejembi alihudumu kama Mkuu wa Wilaya katika Wilaya ya Kongwa. Mheshimiwa Spika, baada ya kuchaguliwa kuwa Mbunge, Mheshimiwa Ndejembi ameendelea kuaminiwa na Mheshimiwa Rais na kupewa majukumu mbalimbali ndani ya Serikali."
"Amehudumu katika nafasi ya Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora; Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa; Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu; Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, kabla ya kuhudumu kama Waziri wa Nishati," ameongeza Waziri Mkuu.
Dkt. Mwigulu amesema katika kipindi ambacho amehudumu ndani ya Serikali, Mheshimiwa Ndejembi ameonesha uwezo wa kubeba majukumu mbalimbali na kufanya kazi katika sekta zenye mahitaji na changamoto zinazotofautiana, akisisitiza kuwa uzoefu huo ni muhimu kwa Makamu wa Rais ambaye, kwa nafasi yake, anatakiwa kuwa tayari kumsaidia Rais katika masuala mbalimbali ya Jamhuri ya Muungano na kutekeleza majukumu yoyote atakayokabidhiwa kwa mujibu wa Katiba.
"Kwa kuzingatia majukumu ya Kikatiba ya Makamu wa Rais niliyoyaeleza, pamoja na uzoefu wa kisiasa, kiutawala na kiutendaji wa Mheshimiwa Deogratius John Pancras Ndejembi, Serikali inaamini kuwa ana uwezo wa kutekeleza kwa uaminifu na ufanisi majukumu ya nafasi ya Makamu wa Rais na kumsaidia Mheshimiwa Rais katika kuendeleza shughuli za Serikali na maendeleo ya Taifa letu," amefafanua Dkt. Mwigulu.



















.jpeg)






.jpeg)

.jpeg)




.jpeg)

.jpeg)


.jpeg)

.jpeg)