WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba ameitaka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia pamoja na taasisi zake kuhakikisha bunifu zinazozalishwa na Watanzania haziishii kuonyeshwa kwenye maonesho, bali zinaendelezwa, zinalindwa na kupelekwa sokoni ili zitoe suluhisho kwa changamoto mbalimbali na kuchangia ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Waziri Mkuu ametoa maelekezo hayo leo, Jumatatu, Agosti 24, 2026, jijini Tanga wakati akihitimisha Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu, akisisitiza umuhimu wa kujenga mfumo unaowawezesha wabunifu kubadilisha mawazo yao kuwa bidhaa na huduma zenye tija.

Amesema Tanzania ina wabunifu wenye uwezo mkubwa katika maeneo mbalimbali, hivyo hatua inayohitajika sasa ni kuhakikisha ubunifu huo unavuka hatua ya kuoneshwa kwenye maonesho na kufikia hatua ya kutumika, kuzalishwa kwa wingi na kuuzwa sokoni.

“Ni lazima tuvuke kwenye maonesho, twende kwenye uhalisia wa maisha kwamba hivi vitu ambavyo tunavionyesha kwenye maadhimisho kama haya sasa viende kwenye utaratibu wa kila siku wa maisha, tuvitengeneze vya kutosha, vitumike na viingie sokoni,” amesema Dkt. Mwigulu.

Aidha, Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kuwekeza katika sayansi, ujuzi na ubunifu kwa lengo la kuyageuza maeneo hayo kuwa nguzo muhimu za uchumi wa Taifa na kuchochea maendeleo kupitia matumizi ya tafiti na teknolojia.

“Hatutaweza kuendelea bila kuwa na sayansi, teknolojia na tafiti na tukatumia matokeo ya tafiti hizo. Hatutapata tija bila kutumia matokeo ya tafiti hizo,” amesema.

Dkt. Mwigulu pia amesema Serikali haitakubali kushusha viwango vya elimu, akisisitiza umuhimu wa taasisi zinazosimamia ubora wa elimu kuendelea kusimamia misingi ya kitaaluma katika kuandaa wataalamu wenye uwezo unaokubalika.

“Tusitengeneze mazingira yawe rahisi ya kujifunza, yawe na alama kubwa kubwa, lakini kazini kuwe na zero kubwa kubwa. Hiyo hapana. Lazima tusimamie misingi ya elimu,” amesema.

Amesisitiza kuwa katika sekta nyeti kama afya, uhandisi na elimu, ubora wa mafunzo haupaswi kuchezewa.

“Hatuwezi kucheza na afya za Watanzania… Hatuwezi tukaandaa wataalamu kwa namna duni duni hivi, tutaharibu sekta yote. Tunataka walimu walio bora, maengineia walio bora; wakijenga daraja, wakijenga jengo, liwe jengo kweli kweli,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameagiza mipango ya maendeleo ya Uwanja wa Ndege wa Tanga iangalie mahitaji ya kiuchumi na kijamii ya mkoa huo kwa kipindi cha miaka 25 ijayo, ili miundombinu inayojengwa sasa iendane na ukuaji wa uchumi, biashara, uwekezaji na ongezeko la matumizi ya usafiri wa anga.

“Lazima tunapojenga tuwaze mbele, tusijenge kwa ajili ya leo. Tuwaze mbele miaka 20 mbele, 25 mbele, kama ambavyo Dira yetu inatuambia,” amesema Dkt. Mwigulu.

Amesema uwanja huo unapaswa kujengwa kwa hadhi ya Tanga kama lango muhimu la shughuli za kiuchumi kutokana na miradi mikubwa inayotekelezwa katika mkoa huo.

Kwa upande wake, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda amesema maonesho hayo yanaakisi jitihada za Serikali katika kutekeleza maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuimarisha elimu inayounganisha nadharia na vitendo, ili kuandaa wahitimu wenye ujuzi wa kujiajiri na kuingia kwa ufanisi katika soko la ajira.

Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Prof. Caroline Nombo amesema jumla ya taasisi 91 za umma na binafsi zimeshiriki katika maadhimisho hayo, ambayo yamehusisha maonesho ya elimu, sayansi, teknolojia na ubunifu, mashindano ya kitaifa ya ujuzi na ubunifu pamoja na makongamano yaliyolenga kujadili mchango wa elimu, ujuzi na teknolojia katika kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo, Mhe Husna Sekiboko amesema Bunge litaendelea kuunga mkono jitihada za Serikali za kuendeleza elimu, ujuzi na ubunifu kupitia bajeti, sera na miongozo inayolenga kuwawezesha watafiti na wabunifu wa ndani kutoa mchango mkubwa katika maendeleo ya Taifa. Amesema kuna umuhimu wa kuzipa kipaumbele bidhaa na teknolojia zinazozalishwa nchini, zikiwemo katika taasisi za Serikali, ili kuongeza matumizi ya bunifu za Watanzania na kuchochea ukuaji wa wabunifu hao.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dkt. Batilda Buriani amesema uwekezaji wa Serikali katika sekta ya elimu umeendelea kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia mkoani humo, kuongeza miundombinu na kuchochea mafanikio ya wanafunzi, huku akipongeza maonesho hayo kwa kuibua na kuonesha uwezo mkubwa wa Watanzania katika sayansi, teknolojia na ubunifu.

Kaulimbiu ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu mwaka 2026 ni “Elimu, Ujuzi na Ubunifu: Njia ya Kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.”









Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Imani kwamba haki inaweza kufuatiliwa na kupatikana bila kujali hali ya mtu imeongezeka kwa familia moja kutoka Meru mkoani Arusha, baada ya kupata msaada kupitia Programu ya “Sema na Waziri” ya Wizara ya Katiba na Sheria.

Familia hiyo ilikuwa imekumbwa na changamoto baada ya kuacha kazi ya ualimu katika shule ya msingi ambako walikuwa wakijitolea kufundisha, huku ikiwa bado inadai stahiki zake. Changamoto hiyo iliwasilishwa kupitia programu hiyo na kuanza kufanyiwa kazi na watumishi wa Wizara.

Ufuatiliaji uliofanywa na Wizara kwa kuwasiliana na wahusika umefanikisha familia hiyo kupata stahiki zilizokuwa zikidaiwa, hatua ambayo imeelezwa kuwa imewapa matumaini mapya kuhusu upatikanaji wa haki.

Akizungumza katika programu hiyo, Lidya Ernest kutoka Meru, Arusha, amesema awali alikuwa na mtazamo kwamba haki ilikuwa rahisi kupatikana zaidi kwa watu wenye uwezo, lakini uzoefu walioupata umebadili mtazamo huo.

“Nitumie nafasi hii kumshukuru Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuweka Programu ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia kwa ajili ya kutusaidia Watanzania wote bila kuangalia matabaka wala nyadhifa, wala hali ya mtu. Hata sisi watu wa huku chini nasi tumefikiwa,” amesema Lidya.

Kwa mujibu wa Lidya, hatua hiyo imewapa yeye na mume wake ujasiri wa kuendelea kufuatilia haki zao kupitia njia sahihi, huku wakitambua umuhimu wa huduma za msaada wa kisheria kwa wananchi wanaokabiliwa na changamoto mbalimbali.

Katika hatua nyingine, Wizara ya Katiba na Sheria imewakabidhi Lidya na mume wake Sh milioni 1.5, fedha zilizotolewa na Rais Samia Suluhu Hassan kwa ajili ya kuwawezesha kuanzisha shughuli za ujasiriamali na kujikwamua kiuchumi.

Msaada huo unalenga kuwapa fursa ya kutumia fedha hizo kama mtaji wa shughuli za uzalishaji, hatua inayotarajiwa kusaidia familia hiyo kujenga chanzo cha kipato na kuimarisha maisha yao.

Tukio hilo limeonyesha pia nafasi ya Programu ya “Sema na Waziri” katika kuwapa wananchi jukwaa la kuwasilisha changamoto zao za kisheria na kupata ufuatiliaji kutoka kwa Wizara.

Kwa familia hiyo kutoka Meru, msaada walioupata haujaishia katika kurejeshewa stahiki walizokuwa wakidai, bali umeenda sambamba na kupata mtaji wa kuanza shughuli za ujasiriamali, jambo ambalo wameeleza kuwa limewapa matumaini mapya ya kujikwamua kiuchumi.

Hatua hiyo pia inaendelea kuimarisha ujumbe kwamba upatikanaji wa haki haupaswi kuwa fursa ya wachache, bali huduma inayopaswa kuwafikia wananchi wote bila kujali uwezo wao, hadhi au nafasi zao katika jamii.


 






Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Rais wa Taasisi ya Maendeleo ya Diaspora wa Kiafrika (ADDI) Balozi Dkt. Arikana Chihombori-Quao, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 24 Agosti, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Rais wa Taasisi ya Maendeleo ya Diaspora wa Kiafrika (ADDI) Balozi Dkt. Arikana Chihombori-Quao baada ya mazungumzo, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 24 Agosti, 2026.




Jumla ya miradi 42 katika mkoa wa Geita, itakaguliwa, kuzinduliwa na kuwekwa mawe ya msingi na mwenge wa uhuru ambao umepokelewa Leo mkoani Geita.

MKUU wa Mkoa wa Geita, Martine Shigela, Agosti 24, 2026 amepokea rasmi Mwenge wa Uhuru kutoka Mkoa wa Shinyanga.

Hafla ya mapokezi imefanyika katika Kijiji cha Nyang'holongo, Kata ya Nundu, Wilaya ya Nyang'hwale.

Akizungumza baada ya kupokea mwenge huo, Mkuu wa Mkoa amesema Mkoa wa Geita kwa mwaka 2026 utakimbizwa katika Halmashauri 6.

Atanzia na Halmashauri ya Nyang'hwale hadi kumalizia katika Halmashauri ya Chato, kwa mujibu wa ratiba iliyopangwa.

Ameeleza kuwa wakati wa ukimbizaji wa Mwenge Mkoani Geita, utakimbizwa kwa umbali wa Kilometa 698.2.

Katika kipindi hicho jumla ya miradi 42 yenye thamani ya Shilingi Bilioni 168.74 itapitiwa. Miradi hiyo itazinduliwa, kuekwa mawe ya msingi, kukaguliwa na kutembelewa.







CRDB Bank imeshiriki katika kilele cha Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu 2026, kinachofanyika Jijini Tanga, ikiwa ni sehemu ya ushiriki wa wadau mbalimbali kutoka sekta ya umma na binafsi katika maadhimisho hayo.

Ushiriki wa CRDB Bank unaendelea kuakisi nafasi ya sekta ya fedha katika kuchangia jitihada zinazolenga kuimarisha elimu, ujuzi na ubunifu kama nyenzo muhimu katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini

John Mtani, Meneja Mwandamizi wa Biashara za Serikali, CRDB Bank, akishiriki katika kilele cha Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu 2026 jijini Tanga, pamoja watumishi, viongozi mbalimbali na wananchi waliotembelea Banda la CRDB Benki.






JUMLA ya wazee 246 wa Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga mkoani Rukwa wamepatiwa vitambulisho vya msamaha wa matibabu hatua inayolenga kuimarisha upatikanaji wa huduma za afya kwa wazee bila vikwazo vinavyotokana na ukosefu wa vitambulisho hivyo.

Akizungumza katika kikao cha Baraza la wazee cha robo ya nne kwa mwaka wa fedha 2025/2026 Afisa Ustawi wa Jamii wa Manispaa ya Sumbawanga Herry Sanga amesema wamefanikiwa kutoa vitambulisho vya msamaha wa matibabu ikiwa wanawake 138, wanaume 108 huku wazee 29 ambao hawakuwa na vitambulisho vya msamaha wa matibabu wamepewa msamaha wa muda wa matibabu.

Kwa upande wake katibu wa Baraza la wazee Manispaa ya Sumbawanga Moris Massanja amesisitiza umuhimu wa kuendelea kutoa elimu kwa wazee kuhusu haki zao pamoja na huduma zinazopatikana kwa ajili yao.

Utoaji wa vitambulisho vya msamaha wa matibabu kwa wazee unalenga kuimarisha upatikanaji wa huduma za afya kwa wazee katika Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga na kuhakikisha wazee wanapata huduma za matibabu kwa wakati na bila vikwazo vinavyotokana na ukosefu wa vitambulisho.



WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amewasili leo Jumatatu, Agosti 24, 2026, katika Uwanja wa Ndege wa Mkoa wa Tanga, ambapo anatarajiwa kuwa Mgeni Rasmi katika kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanayofanyika katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara, mkoani Tanga.

Amepokelewa na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Batilda Burian, pamoja na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Prof. Adolf Mkenda.

Alipowasili katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara, Waziri Mkuu ametembelea mabanda mbalimbali ya maonesho na kujionea bunifu, teknolojia na kazi mbalimbali zinazowasilishwa na washiriki katika maadhimisho hayo.








Na Mwandishi Wetu, Tanga
MKURUGENZI Mkuu wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), CPA Anthony Kasore, amesema mamlaka hiyo imeweka mkakati wa kutoa mafunzo ya ufundi na ujuzi kwa vijana ili kuwafungulia fursa za ajira na kujiajiri katika sekta mbalimbali.

CPA Kasore ameyasema hayo alipotembelea Banda la VETA katika Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara jijini Tanga.

Amesema VETA ina vyuo katika mikoa mbalimbali nchini, hivyo vijana wanapaswa kutumia fursa hiyo kujiunga na vyuo hivyo na kupata ujuzi unaowawezesha kukabiliana na mahitaji ya soko la ajira.

“VETA imejenga vyuo katika kila mkoa na wilaya zake kwa kuzingatia mahitaji ya wananchi wa maeneo husika, ili kuhakikisha changamoto zao zinapatiwa ufumbuzi kupitia elimu na mafunzo ya ufundi stadi,” amesema CPA Kasore.

Aidha, amesema gharama za mafunzo kwa wanafunzi wanaosoma kozi ndefu ni Sh 60,000 kwa mwaka kwa wanafunzi wa kutwa, huku wanafunzi wa bweni wakilipia Sh 120,000 kwa mwaka.

Amesema gharama hizo zimewekwa ili kuwawezesha vijana wengi kupata fursa ya elimu na mafunzo ya ufundi stadi bila kukwamishwa na gharama kubwa.

CPA Kasore amesema kupitia vyuo vyake, VETA imekuwa ikikuza ubunifu katika sekta mbalimbali kwa lengo la kutatua changamoto zinazowakabili wananchi pamoja na kurahisisha shughuli zao katika mazingira bora.

Amesema ubunifu huo ni sehemu ya juhudi za VETA kuhakikisha vijana wanapata ujuzi unaoendana na mahitaji ya sasa na kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi, ajira na kujiajiri.



Na Mwandishi Wetu, Tanga
WANAFUNZI wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere (MNMA) wamebuni mifumo ya kidijitali inayolenga kurahisisha usimamizi wa taka na matumizi ya maji kwa kutumia teknolojia ya mawasiliano.

Mwanafunzi wa Fani ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT), Fatuma Ismail, amebuni mfumo unaowezesha vifaa vya kuhifadhi taka kutoa taarifa kwenye simu janja pindi taka zinapofikia kiwango cha kujaa, hivyo kurahisisha hatua za kuziondoa.

Akizungumza katika Banda la MNMA kwenye Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara jijini Tanga.

Fatuma amesema mfumo huo unalenga kusaidia katika utunzaji wa mazingira na kudumisha usafi.

Amesema mfumo huo unaweza kutumiwa katika maeneo mbalimbali, ikiwemo majumbani, kwa kufungwa kwenye vifaa vya kuhifadhi taka ili kutoa taarifa kwa njia ya simu janja pindi taka zinapokuwa zimejaa.

Fatuma amesema mfumo huo pia unaweza kusaidia Baraza la Taifa la Usimamizi na Uhifadhi wa Mazingira (NEMC) kufuatilia hali ya maeneo ya kuhifadhi taka na kupata taarifa kwa wakati ili kuchukua hatua stahiki.

Amesema matumizi sahihi ya mfumo huo yanaweza kupunguza msongamano wa taka katika maeneo mbalimbali kutokana na kuwepo kwa mawasiliano ya moja kwa moja kati ya kifaa cha kuhifadhi taka na mtumiaji.

Kwa upande mwingine, mbunifu wa MNMA, Godfrey Kasembe, amebuni kifaa kinachoweza kufungwa kwenye mita za maji na kutoa taarifa za matumizi ya maji moja kwa moja kwenye simu janja au kompyuta bila mhusika kwenda kusoma mita hizo.

Kasembe amesema MNMA imekuwa ikimsimamia kwa karibu katika hatua zote za ubunifu huo, kuanzia wazo hadi kufikia hatua ya kutengeneza kifaa.

Amesema mfumo huo utasaidia mamlaka za maji kupunguza gharama na muda unaotumika kwa watumishi kwenda nyumba kwa nyumba kusoma mita, kwa kuwa taarifa za matumizi zitapatikana moja kwa moja kupitia mfumo huo.

Ameongeza kuwa teknolojia hiyo pia itasaidia kupunguza uwezekano wa udanganyifu katika usomaji wa mita kwa kuwa taarifa za matumizi zitakuwa zikiwasilishwa moja kwa moja kwenye mfumo. Kasembe amesema kwa sasa mfumo huo upo katika hatua za usajili ili kukamilisha taratibu na kuanza kutumika.



Na Mwandishi Wetu, Tanga
CHUO cha Elimu ya Biashara (CBE) kimesema kimeweka mfumo wa kuwawezesha wanafunzi kuendeleza mawazo na bunifu zinazolenga kutoa suluhisho kwa changamoto zinazowakabili wananchi.

Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Masoko wa CBE, Georgina Misama, amesema hayo kwenye Banda la chuo hicho katika Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea jijini Tanga.

Amesema kupitia wiki hiyo, CBE imekuwa ikitoa elimu kwa wananchi pamoja na kuonyesha bunifu mbalimbali zinazozalishwa na wanafunzi, huku chuo kikiwasimamia wanafunzi kuanzia hatua ya awali ya wazo hadi kukamilika kwa bunifu hizo.

“Chuo kimekuwa na mfumo wa kuendeleza bunifu na mawazo yanayotolewa na wanafunzi ambayo yana lengo la kutatua changamoto zinazowakabili wananchi,” amesema Georgina.

Kwa upande wake, mwanafunzi wa mwaka wa tatu wa CBE, Amiri Sharifu, amebuni kifaa cha kidijitali kwa ajili ya wakaguzi wa mizani, kinachowawezesha kupata taarifa za mizani wanayoikagua moja kwa moja kupitia simu zao za mkononi.

Amesema mfumo huo unalenga kuondoa changamoto ya wakaguzi kutembea na vitabu vya karatasi nyingi wakati wa kujaza taarifa za ukaguzi wa mizani, huku pia ukipunguza muda unaotumika katika zoezi hilo.

“Kwa kutumia mfumo huu, mkaguzi anaweza kupata taarifa za mzani papo hapo kupitia simu yake ya mkononi bila kutegemea karatasi, jambo ambalo litasaidia kupunguza muda wa ukaguzi,” amesema Sharifu.

Naye mwanafunzi wa mwaka wa kwanza, Sambu Timothy, amebuni mfumo wa kidijitali unaojulikana kama Smart Mauzo, unaomsaidia mfanyabiashara kupata taarifa za mauzo ya biashara yake kupitia simu janja.

Amesema mfumo huo una uwezo wa kutambua wateja ambao hawajafanya manunuzi kwa muda mrefu na kuwawezesha wafanyabiashara kuwatumia ujumbe mfupi wa simu (SMS) ili kuwakumbusha kuhusu bidhaa au huduma zao.

Timothy amesema mfumo huo upo katika hatua za mwisho za kukamilishwa na baada ya hapo utaingizwa sokoni kwa lengo la kuwasaidia wafanyabiashara kutunza kumbukumbu za uwekezaji, mauzo na matumizi, hatua ambayo itawasaidia kukuza biashara zao.





Na Mwandishi Wetu, Tanga
MAMLAKA ya Elimu Tanzania (TEA) imesema mdau yeyote atakayechangia katika Mfuko wa Elimu wa Taifa, ataweza kupata fursa ya kuomba nafuu ya kodi kwa kutumia cheti cha utambuzi kinachotolewa na mamlaka hiyo.

Akizungumza katika Banda la TEA kwenye Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara jijini Tanga, Afisa Mwandamizi wa TEA Joyce Minja amesema, wachangiaji wa Mfuko wa Elimu hupata manufaa mbalimbali kutokana na mchango wao katika kuendeleza sekta ya elimu.

Amesema miongoni mwa manufaa hayo ni kutambuliwa kwa mchango wao, kupata fursa ya kuomba nafuu ya kodi pamoja na kutangazwa ndani na nje ya nchi kama sehemu ya kuhamasisha wadau wengine kushiriki katika maendeleo ya elimu.

“Wachangiaji wa Mfuko wa Elimu wa Taifa, watapewa Cheti au Barua ya utambuzi wa uchangiaji elimu katika kusaidia maendeleo na uboreshaji miundombinu ya sekta ya elimu,” amesema Minja.

Ameongeza kuwa, cheti hicho kinaweza kutumika katika kuomba nafuu ya kodi kwa mujibu wa Kifungu cha 16(1) cha Sheria ya Kodi ya Mapato, Sura ya 332, Toleo la 2019.

Aidha, amesema wachangiaji wataingizwa katika kanzidata ya wachangiaji wa Mfuko wa Elimu, hatua itakayosaidia kutunza kumbukumbu zao kwa kudumu na kuwezesha kutambua mchango walioutoa katika sekta ya elimu.

Kwa mujibu wa TEA, wachangiaji pia watapata fursa ya kutambuliwa na kutangazwa ndani na nje ya nchi, ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha ushiriki wa wadau katika kusaidia maendeleo ya elimu.

Mfuko wa Elimu wa Taifa unalenga kuimarisha ushiriki wa wadau mbalimbali katika maendeleo ya sekta ya elimu kupitia michango na misaada inayolenga kuboresha mazingira na huduma za elimu nchini.

Amewataka wadau mbalimbali ,wakiwemo wafanyabiashara ,wenye viwanda ,Taasisi za Serikali, Sekta Binafsi mashirika ya ndani na nje ya nchi kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali za kuboresha miundombinu ya kujifinzia na kufundishia kwa kuchangia rasilimali fedha au vifaa kupitia Mfuko huo wa Elimu wa Taifa

Top News