Mkutano wa 6 wa Serikali Mtandao umemalizika Februari 19, 2026, huku Halmashauri ya Wilaya ya Geita ikitangazwa kuwa Mshindi Namba Moja kati ya Halmashauri 184 nchini katika matumizi bora ya mifumo ya kiserikali kwa kuzingatia sheria, viwango na miongozo inayotolewa na Mamlaka ya Serikali Mtandao.

Tuzo hiyo imetolewa katika Mkutano wa 6 wa Serikali Mtandao uliofanyika katika ukumbi wa Arusha International Conference Centre (AICC), jijini Arusha na kukabidhiwa na Mhe Ridhiwani Kikwete, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wakati akifungua Kikao hicho cha 6.

Mkutano huo wa siku 3, ulifunguliwa rasmi Februari 17, 2026 na Mhe Moses Mpogole Kusiluka, Katibu Mkuu Kiongozi (KMK) ambapo amesema Nchi ya Tanzania ipo katika muelekeo sahihi wa mageuzi ya kidijitali. "Mimi naiona Tanzania nzuri sana wala sio baadaye sana ni hivi Karibuni" Amesema Balozi Dkt Kusiluka.

Vile Vile Katibu Mkuu Kiongozi amesema Serikali imewekeza kwa kiasi kikubwa kwenye TEHAMA na hii ni kwa kutambua kuwa maendeleo ya sasa hayawezi kupatikana nje ya mifumo ya kidijitali.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri, Karia Magaro, ameishukuru Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGa) kwa kutambua juhudi hizo, na amekipongeza Kitengo cha TEHAMA kwa usimamizi madhubuti wa mifumo ya kiserikali inayowezesha utoaji wa huduma bora kwa wananchi.

"Tuendelee kujikita kwenye mifumo na kuongeza kasi katika mifumo yote inayoletwa na Serikali" Amesema Magaro.

Naye Mkuu wa Kitengo Cha TEHAMA, Halmashauri ya Wilaya ya Geita Frank Makonda ametoa rai kwa watumishi wa Halmashauri kuendelea kushirikiana na kuongeza bidii kwenye ubunifu wa kutoa huduma kwa wananchi kwa kufuata Sheria na miongozo inayotolewa na Mamlaka ya Serikali Mtandao.

Ushindi Huo wa Tuzo hiyo (Best Performance in Compliance to e-Government Act, Standards and Guidelines) ni ushahidi kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Geita chini ya Mkurugenzi Mtendaji Karia Rajab Magaro, inaongoza kwa ubunifu, uwazi na matumizi sahihi ya TEHAMA katika utumishi wa umma.

Kikao hicho kimeongozwa na Kauli Mbiu isemayo " Kuboresha utendaji wa Serikali kwa kuimarisha utoaji wa huduma za umma kupitia mifumo salama na Jumuishi ya Serikali Mtandao.







Leo tarehe 20.2.2025 Mkuu wa mkoa wa Rukwa. Mhe. Makongoro Nyerere ametembelea Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) na kuwasilisha pongezi zake kuwa Tangu kuanzishwa kwake TADB ni benk ambayo imekuwa kwa kasi kubwa ndani ya miaka kumi (10) ikihudumua wakulima, wafugajo na wavuvi ambao mkoani Rukwa wapo na wanategemea mikopo ya benki hii kwa masharti ya riba nafuu.

Akipokea ugeni huo Bw. Frank Nyabundege Amempongeza Mhe. RC kwa kuaminiwa na kuteuliwa na Mhe Rais kuwa mkuu wa mkoa wa Rukwa.

Aidha amemuelezea kuwa mafanikio ya Benk ya TADB yametokana na jitihada za Serikali awamu ya sita inayoongozwa na Mhe.Dkt Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania kuiongezea benk fedha katika mtaji wa benki ili kufikia wakulima, wafugaji na wavuvi wengi hapa nchini.


Leo tarehe 20.2.2026 Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo ya kilimo Tanzania (TADB) Bw. Frenk Nyabundege amepokea ujumbe wa TANZANIA NATIONAL CHAMBER OF COMMERCE ukiongozwa na Bw.Painetho Madembwe akiambatana na wawakilishi toka TNCC makao makuu pamoja na AGGOT waliotembelea katika ofisi za TADB makao makuu kinondoni jijini dar es salaa.

Lengo la ugeni huo ni kukabidhi Tuzo ya shukrani kwa TADB kufanikisha na kuchagiza maendeleo ya biashara za kilimo mkoani iringa Na kuwezesha Mikopo yenye kusaidia ustawi wa kilimo cha chai, kahawa,parachichi na mahindi huko kilolo mkoani iringa.

Akipokea tuzo hiyo Bw. Nyabundege amewahakikishia kuwa benki yao itaendelea kutoa huduma za kifedha kwa wakulima na wafugaji katika mikoa yote na kuchagiza kilimo kuleta mtazamo wa kilimo biashara ambacho kinabenkika kwa maslahi ya ustawi wa wakulima na uchumi wa nchi.




Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Jakaya Kikwete, ameweka jiwe la msingi la ujenzi wa chuo cha Utumishi wa Umma Kampasi ya Tanga, leo tarehe 20 Februari 2026. 

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mheshimiwa Kikwete amethibitisha kuwa serikali imeamua kutumia kiasi cha shilingi bilioni 39 kwa ajili ya ujenzi wa kampasi hiyo, fedha zitakazotengwa kila mwaka hadi kukamilika kwa mradi mzima.
 
 “Namshukuru sana Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samaia Suluhu Hassan kwa kukubali na kuruhusu kutenga kiasi cha shilingi Bill 39 za ujenzi wa Kampasi ya Tanga” amesema Mhe. Kikwete. 
Aidha, amesisitiza ujenzi wa mradi wa kampasi ya Tanga unatokana na elimu kuwa kipaumbele na kusisitiza kuwa serikali   itaendelea kuwekeza katika elimu na kuhakikisha utumishi wa umma unaboreshwa nchini ambalo ni jukumu la chuo kuwajengea uwezo watumishi wa umma nchini.

Pia Mhe. Kikwete amesema kuwa, ameridhishwa na kiwango cha kazi kilichofanyika na kuipongeza menejimenti ya chuo kwa kusimamia kwa makini ujenzi wa kampasi. Amesema kuwa ujenzi huu unalenga kuimarisha huduma za utumishi wa umma nchini kupitia kampasi itakayojenga mustakabali mzuri wa elimu na utumishi bora.

    Akitoa taarifa ya mradi wa ujenzi, Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, Dkt. Ernest Mabonesho amesema kuwa awamu ya kwanza ya ujenzi ilianza rasmi tarehe 8 Februari 2025, ikiwa ni ujenzi wa jengo la ghorofa mbili la  madarasa gharama za takriban shilingi bilioni 6.16. 

Dkt. Mabonesho amesema kua, Jengo litajumuisha madarasa 26 yatakayohudumia zaidi ya wanafunzi 2,500 kwa awamu moja, ofisi 24 za watumishi, kumbi mbili za mikutano, na vyoo vya kisasa 18. Vilevile, amesema jengo hili litakuwa na miundombinu ya kisasa ya TEHAMA itakayowezesha matumizi ya teknolojia katika kufundisha, kujifunza, na kuendesha shughuli za kitaaluma kwa ufanisi zaidi.

Dkt. Mabonesho pia alibainisha kuwa mradi huu utaleta manufaa makubwa kwa wananchi kiuchumi kutokana na huduma zitakazotolewa na chuo, ikiwemo kuimarisha ajira na maendeleo ya kijamii. Ujenzi huu unaonyesha dhamira ya serikali ya kuimarisha sekta ya elimu na utumishi wa umma nchini, na kuleta maendeleo zaidi kwa mkoa wa Tanga na taifa kwa ujumla.

Mradi wa ujenzi wa Kaampasi ya Tanga unatekelezwa katika eneo la hekari 14 lililopo Kange Uzunguni, mjini Tanga. Awamu ya kwanza ya ujenzi ilianza rasmi tarehe 8 Februari 2025,













 

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amekutana na kufanya mazugumzo na Balozi wa India nchini Tanzania Mhe. Bashwadip Dey, mazungumzo yaliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 20 Februari 2026.

Mazungumzo hayo, yamelenga kuimarisha zaidi ushirikiano baina ya India na Tanzania katika sekta mbalimbali za kimkakati. Mahusiano kati ya nchi hizi mbili yamejikita katika sekta ya Afya, Maji, Elimu,Biashara na Uwekezaji pamoja masuala ya Ulinzi na Usalama.

Tanzania na India zina mahusiano mazuri ya kidiplomasia yaliyoanza baada ya Tanzania kupata uhuru ambapo India ilifungua Ubaozi wake mwaka 1961 na Tanzania kufungua Ubalozi wake nchini India mwaka 1962.

Mwaka 2023 mahusiano kati ya nchi hizi mbili yaliongezeka zaidi na kuwa mahusiano ya kimkakati kufuatia ziara rasmi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, aliyoifanya nchini India.

India imekuwa na mchango mkubwa katika miradi mbalimbali ya maji inayotekelezwa na Serikali pamoja na kutoa mchango mkubwa katika sekta ya Afya ikiwemo utoaji wa huduma za afya nchini, mafunzo pamoja na Vifaa Tiba.

India imekuwa mdau muhimu wa biashara nchini Tanzania ambapo hadi sasa inashika nafasi ya tatu duniani kwa kufanya biashara na Tanzania. Bidhaa ambazo Tanzania inauza zaidi nchini India ni pamoja na Korosho, karanga, mboga za jamii ya kunde, vito vya thamani na vito vya thamani, pamba; karafuu, chai, Ngozi, mbao na bidhaa za mbao.









Na Mwandishi Wetu

Watumiaji wa gesi ya kupikia wamepata nafuu baada ya Oryx Gas Tanzania kuzindua kampeni ya “Pishi la Kibabe” kwa Ramadhan na Kwaresma, itakayoshusha bei ya mtungi mpya wa kilo sita hadi Sh. 37,000 nchi nzima.

Akizungumza leo Februari 20,2026 jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi huo Meneja Masoko na Mauzo wa Oryx Gas Tanzania Shaban Fundi amesema huu ni mwezi wa kujitafakari ,kushirikiana ,kujitolea na zaidi ya yote kuunganisha watu wote.

“Ili kuunga mkono wateja wetu katika kipindi hiki maalum tunatoa bei ya promosheni kwenye mitungi yetu mipya ya kilo sita itauzwa kwa Sh.37000 nchi nzima hadi Zanzibar.”amesema Fundi

Pia amesema mbali ya kupunguza bei katika kipindi hiki cha Ramadhan na Kwaresma wateja wao watakaonunua au kujaza gesi kwenye maduka maalum ya Oryx na Mangi Shop watapokea zawadi ya futari papo kama ishara ya shukrani yao kwao.

Akizungumza kuhusu gharama za mtungi wa kilo sita amesema mpaka unafika nchini Tanzania gharama yake haipungui Sh.80,000 lakini Oryx katika soko mtungi huo unapatikana kwa Sh.40000 na kwa sasa tumetoa promosheni mpaka Sh.37000.

-“Hata hivyo tunaomba Serikali iendelee kuangalia katika maeneo mengine ili kuhakikisha kwamba gesi pamoja na mtungi bei yake inakuwa chini ili wananchi waweze kupata kwa bei nafuu.Kwafanya hivyo Oryx Gas kwa kushirikiana na Serikali tunaweza kufanikisha matumizi ya nishati safi kwa wananchi wengi zaidi.”

“Kuhusu gharama ukilinganisha mkaa na kuni bei yake iko juu zaidi ya nishati safi ya kupikia kwani kwa familia ya kawaida kwa siku moja inatumia kopo moja la mkaa ambalo linauzwa Sh.2000 hivyo kwa mwezi ni Sh.60,000 wakati mtungi wa gesi ya oryx wa kilo 6 ni Sh.40,000.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Oryx Gas Tanzania Benoit Araman amesema lengo la kampeni iliyozinduliwa kwa ajili ya Mfungo wa Mwezi wq Ramadhan na Kwaresma ni muendelezo wa kuhamasisha matumizi ya nishati safi nchini ikiwa ni kuunga mkono juhudi za Serikali za kuhimiza wananchi kutumia nishati safi ya kupikia.

“Oryx Gas lengo letu kubwa ni kuendelea kuhamasisha nishati safi ya kupikia na mimi na timu yangu tumejipanga vema kuhakikisha tunaendelea kufanya kampeni za kuwezesha wananchi kutumia nishati safi ya kupikia.Wakati huu wa Ramadhan na Kwaresma tunawatakia mfungo mwema lakini wakati huo huo tukihamasisha matumizi ya nishati safi.”

Wakati huo huo Mkuu wa Idara ya Mauzo ya Gesi kwa Ujumla Carloline Msokwa amesema kipindi hiki Waislamu na Wakristo wanaungana pamoja kuomba toba na ni kipindi ambacho familia zinakaa kufanya ibada na kuomba toba lakini pia ni wakati wa kupika chakula kizuri kwa ajili ya kufuturu.

“Kwahiyo Oryx Gas tumekuja na kampeni ya Pishi la kibabe ambapo familia zitakaa na kupika pamoja lakini pia Oryx tumetoa punguzo la bei ili kuwezesha wananchi kutumia gesi.Pia nitoe rai huu ni wakati wa Watanzania kuwa wamoja na tuliombee taifa letu.”





Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Kanda ya Kati, Dodoma, Dkt. Japhet Nkangaga (kushoto), akipokea changamoto mbalimbali zinazowakabili wafugaji kutoka kwa muuzaji wa pembejeo za mifugo Manispaa ya Singida, Bi. Ester Munuo, tarehe 19 Februari 2026 mkoani Singida, wakati wa ziara ya uhamasishaji kwa wauzaji wa pembejeo za mifugo iliyolenga kutoa elimu kuhusu matumizi sahihi ya chanjo ya Matone (TEMEVAC) na taratibu za upatikanaji wa leseni za uuzaji wa viuatilifu vya rejareja na jumla.


*************


Na Daudi Nyingo – Singida

Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) imeendelea kuimarisha juhudi za kulinda afya ya mifugo nchini kwa kutoa elimu kwa wauzaji wa pembejeo za mifugo mkoani Singida kuhusu utoaji na matumizi sahihi ya chanjo za mifugo zinazozalishwa na taasisi hiyo. 

Zoezi hilo lililofanyika tarehe 19 na 20 Februari 2026 lililenga kuwajengea uwezo wauzaji wa pembejeo kama kiungo muhimu cha kuwafikia wafugaji, ili waweze kutoa elimu sahihi kuhusu utambuzi wa chanjo za TVLA, namna bora ya kuzitunza, matumizi sahihi na umuhimu wa kufuata taratibu za kitaalamu katika utoaji wa chanjo.

Akizungumza wakati wa kuhitimisha zoezi hilo tarehe 20 Februari 2026, Meneja wa TVLA Kanda ya Kati Dodoma, Dkt. Japhet Nkangaga, alisema kuwa ziara hiyo ililenga kutoa elimu kwa wauzaji wa pembejeo na wafugaji kuhusu matumizi sahihi ya chanjo ya Matone (TEMEVAC), ikiwemo namna bora ya kuzipokea, kuzihifadhi katika ubaridi unaostahili ili kudumisha ubora wake na kuhakikisha chanjo zinatumika kwa ufanisi unaokusudiwa.

“Tunasisitiza matumizi sahihi kuanzia hatua ya kufungua chupa ya chanjo. Kama imeandikwa kuwa na dozi 100, ni lazima itoe dozi 100. Endapo tundu litatobolewa kubwa, kunakuwa na uwezekano wa chanjo kutoka nyingi zaidi na kusababisha dozi zilizokusudiwa kutotimia,” alisema Dkt. Nkangaga.

Aliongeza kuwa elimu hiyo pia inahusisha matumizi sahihi ya chanjo baada ya kufunguliwa, akieleza kuwa kuku mmoja hupatiwa tone moja la chanjo na kurudiwa kuchanjwa baada ya miezi mitatu, utaratibu unaoendelea kwa mwaka mzima hadi kuku anapofikia hatua ya matumizi ya binadamu.

Baadhi ya wauzaji wa pembejeo za mifugo mkoani Singida wameibua changamoto ya upatikanaji wa chanjo mbalimbali, hali ambayo imekuwa ikiwalazimu wakati mwingine kupata chanjo kutoka vyanzo visivyo na uhakika. Wameshauri TVLA kuimarisha upatikanaji wa chanjo ili kuhakikisha wauzaji na wafugaji wanapata bidhaa salama, zenye ubora na kutoka katika vyanzo vinavyoaminika, hatua itakayosaidia kudhibiti tatizo la chanjo zisizo halali sokoni.

Bi. Ester Munuo, muuzaji wa pembejeo za mifugo mkoani humo, alisema kuwa pamoja na chanjo ya Newcastle (TEMEVAC), kuna umuhimu wa TVLA kuongeza uzalishaji wa aina nyingine za chanjo za kuku, zikiwemo chanjo za gumboro na ndui, ili kuwapa wauzaji uhakika wa chanzo sahihi cha chanjo.

“Tunapopata chanjo kutoka mamlaka moja inayoaminika, inatusaidia kuepuka kuchukua chanjo kutoka vyanzo visivyo na uhakika, jambo ambalo linaweza kuleta changamoto kwa mtumiaji na kuathiri imani ya wafugaji,” alisema.

Kwa upande wake, Bw. Anthony Ntobi alisema kuwa upatikanaji wa chanjo kwa wakati na kupitia mamlaka rasmi utarahisisha kazi ya wauzaji na kuongeza ufanisi kwa wafugaji.

“Kuna baadhi ya chanjo za kuku ambazo wakati mwingine husambazwa kwa nyakati tofauti. Kupata chanjo moja kwa moja kutoka mamlaka husika kutarahisisha upatikanaji, kupunguza hatari ya chanjo feki na kutuwezesha kuwahudumia wafugaji kwa ufanisi zaidi,” alisema.

TVLA imeeleza kuwa itaendelea kutoa elimu kwa umma na wadau wa sekta ya mifugo katika mikoa mbalimbali nchini kama sehemu ya mkakati endelevu wa kitaifa wa kuimarisha afya za mifugo, kuongeza uzalishaji na kuchangia maendeleo ya sekta ya mifugo nchini.
Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Kanda ya Kati, Dodoma, Dkt. Japhet Nkangaga (kushoto), akitoa elimu kwa muuzaji wa pembejeo za mifugo Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni, Bi. Stella Kahimba, kuhusu taratibu za upatikanaji wa leseni za uuzaji wa viuatilifu vya rejareja na jumla, wakati wa ziara ya uhamasishaji kwa wauzaji wa pembejeo za mifugo iliyofanyika tarehe 20 Februari 2026 mkoani Singida.
Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Kanda ya Kati, Dodoma, Dkt. Japhet Nkangaga (wa pili kutoka kulia), akitoa elimu kwa muuzaji wa pembejeo za mifugo Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni, Bi. Zainabu Ayubu (wa pili kutoka kushoto), kuhusu matumizi sahihi ya chanjo ya Matone (TEMEVAC), ikiwemo namna bora ya kuzipokea, kuzihifadhi na kuzitumia kwa ufanisi, wakati wa ziara ya uhamasishaji iliyofanyika tarehe 20 Februari 2026 mkoani Singida. Wa kwanza kushoto ni Bw. Charles Wambula Afisa Mifugo Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni.
Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Kanda ya Kati, Dodoma, Dkt. Japhet Nkangaga (kulia), akitoa elimu kwa muuzaji wa pembejeo za mifugo Halmashauri ya Wilaya ya Itigi, Bi. Dorcus Sumary, kuhusu matumizi sahihi ya chanjo ya Matone (TEMEVAC) pamoja na taratibu za upatikanaji wa leseni za uuzaji wa viuatilifu vya rejareja na jumla, wakati wa ziara ya uhamasishaji iliyofanyika tarehe 20 Februari 2026 mkoani Singida.
Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Kanda ya Kati, Dodoma, Dkt. Japhet Nkangaga (katikati), akitoa elimu kwa muuzaji wa pembejeo za mifugo Halmashauri ya Wilaya ya Itigi, Bw. Sifael Marko (kushoto), kuhusu matumizi sahihi ya chanjo ya Matone (TEMEVAC) pamoja na taratibu za upatikanaji wa leseni za uuzaji wa viuatilifu vya rejareja na jumla, wakati wa ziara ya uhamasishaji iliyofanyika tarehe 20 Februari 2026 mkoani Singida.

Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Kanda ya Kati, Dodoma, Dkt. Japhet Nkangaga, akitoa elimu kwa muuzaji wa pembejeo za mifugo Manispaa ya Singida, Bw. Abeid Hassan, kuhusu taratibu za upatikanaji wa leseni za uuzaji wa viuatilifu vya rejareja na jumla, wakati wa ziara ya uhamasishaji kwa wauzaji wa pembejeo za mifugo iliyofanyika tarehe 19 Februari 2026 mkoani Singida.
*Ni za wakulima wa kahawa AMCOS ya Mwika Kinyamvuo

*Akagua ujenzi wa hospitali ya Halmashauri ya Manispaa ya Moshi

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amemuagiza Mrajisi wa Vyama vya Ushirika mkoa wa Kilimanjaro ahakikishe Chama cha Ushirika Mkoa wa Kilimanjaro (KNCU) kinalipa kwa mkupuo mmoja sh. milioni 400 ambazo chama hicho kinadaiwa na wakulima.

Ametoa agizo hilo leo (Ijumaa, Februari 20, 2026) aliposimama kusalimia wananchi katika eneo la Chekereni ambapo mkazi wa eneo hilo, Bi. Glory Sam kutoka Chama cha Mwika Kinyamvuo AMCOS alieleza malalamiko yake mbele ya Waziri Mkuu akitaja kusikitishwa na KNCU kuuza kahawa yao msimu wa mwaka 2021/2022 lakini hadi sasa hawajalipwa.

“Tuliuza kahawa yetu kwa zaidi ya shilingi milioni 600 lakini mpaka sasa tumelipwa shilingi milioni 200 pekee. Kwa kipindi chote hicho tumekuwa tukidai milioni 400 bila mafanikio.”

Dkt. Mwigulu amemtaka Mrajis ahakikishe kuwa hadi kufikia tarehe 25 Februari, 2026 Bodi hiyo iwe imekaa kikao na iamue ni mali gani zinauzwa ili kuweza kuwalipa kwa mkupuo wakulima hao.

“Tafuta kimojawapo kiuzwe, shilingi milioni 400 ipatikane na hawa watu walipwe mara moja. Hatuwezi kukaa na jambo moja miaka yote, kama kuna chama hakiwezi kulipa watu mnakaa nacho cha nini? Wananchi wanaumia, tabia ya kuzoea shida, matatizo na machozi ya watu hatuwezi kuivumilia.”

“Jambo limekaa miaka mitano mnataka likae miaka mingapi, upuuzi huu sitaki kusikiliza mnalipa lini? Jumatano ijayo mkae mtoke na majibu, tafuteni mtakachouza muwalipe watu pesa zao,” amesisitiza.

Wakati huohuo, Waziri Mkuu amekagua mradi wa ujenzi wa hospitali ya Halmashauri ya Manispaa ya Moshi inayojengwa katika Kata ya Ng’ambo kwenye manispaa hiyo.

Mradi huo ambao hadi kukamilika kwake unatarajiwa kugharimu sh. bilioni 6.59, hadi sasa ujenzi wake umefikia asilimia 55 ya katika majengo ya huduma za wagonjwa wa nje, huduma za mama na mtoto kwa miundombinu ya sakafu ya chini na ya kwanza.


MKUU wa Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA), Prof. Eliamani Sedoyeka, amesema vijana wengi wanashindwa kufanikiwa katika kujiajiri si kwa kukosa taaluma, bali kwa kukosa maarifa mapana ya uendeshaji wa biashara.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Ijumaa, Februari 20, 2026, Mtumba jijini Dodoma, Prof. Sedoyeka alieleza kuwa pamoja na vijana wengi kuwa na ubunifu na ujuzi katika fani mbalimbali kama teknolojia na utoaji huduma, changamoto huanza wanapokutana na masuala ya fedha na usimamizi.

Alifafanua kuwa ukosefu wa uelewa wa upangaji wa bajeti, usimamizi wa mapato na matumizi, pamoja na mbinu za kuongoza rasilimali watu, umekuwa kikwazo kikubwa kwa ukuaji na uimara wa biashara za vijana.

“Wapo vijana wenye mawazo mazuri na bidhaa zenye ubora, lakini wanaposhindwa kusimamia fedha na mifumo ya kiutawala, biashara zao hushindwa kudumu,” alisisitiza.

Kwa mujibu wake, biashara nyingi huanzishwa kwa ari na matumaini makubwa, lakini hukosa misingi imara ya kiutawala na kifedha inayoweza kuziwezesha kukua na kushindana sokoni.

Akizungumzia suluhisho, Prof. Sedoyeka alisema IAA imeandaa mkakati wa kitaaluma kupitia programu ya “Degree 360”, unaolenga kuwajengea wanafunzi uelewa jumuishi unaohusisha masuala ya fedha, uongozi, usimamizi wa rasilimali watu na mikakati ya biashara.

Alisema lengo la programu hiyo ni kuwaandaa vijana kuwa na uwezo wa kuanzisha na kuendesha miradi au taasisi kwa ufanisi na uendelevu.

Aidha, aliwahimiza vijana kutambua kuwa mafanikio katika kujiajiri yanahitaji zaidi ya kipaji au taaluma pekee; yanahitaji nidhamu ya kifedha, uongozi bora na maarifa sahihi ya biashara.




Top News