Uongozi wa Mamlaka ya Hifadhi ya eneo la Ngorongoro (NCAA) umeeleza kuwa, umedhamiria kuendelea kuboresha utoaji huduma kwa watalii kwa njia za kisasa kupitia matumizi ya teknolojia ya habari na mawasiliano ili kuongeza ufanisi na kasi ya utendaji kazi na ukusanyaji wa mapato.

Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa uhifadhi anayesimamia huduma za Utalii na Masoko Mariam Kobelo ameeleza kuwa lengo la kufanya kazi kidigitali ni kuhakikisha kuwa watoa huduma katika sekta ya utalii wanatumia muda mfupi kuingia na kutoka ndani ya hifadhi pamoja na kuhakikisha maduhuli ya serikali yanakusanywa kikamilifu na kuimarisha usalama wa hifadhi na rasilimali zilizopo.

“Siku mbili zilizopita tumekuwa na changamoto ndogo ndogo katika lango kuu la Ladoure ,tunaendelea kuzitatua kwa ushirikiano mkubwa na wadau wetu”,amesema bi.Kobelo.

Amewashukuru waongoza watalii wote na wadau katika sekta hiyo kwa kuonesha ushirikiano wa kutosha katika kufanikisha maboresho hayo.

Ameongeza kuwa mteja yeyote atakayekutana na changamoto za kiutendaji katika kipindi hiki ni vema akawasiliana na maafisa wa mamlaka hiyo ambao wapo katika lango hilo na maeneo mengine na watasaidiwa ili waweze kuendelea na safari zao kwa muda kama walivyopanga.

Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro katika mwelekeo wa utendaji wake mpya imedhamiria kuimarisha shughuli zake za kutoa huduma bora kwa watalii katika viwango vya kimataifa na kuendelea kuimarisha dawati la huduma na ukarimu kwa wateja.










Serikali imeutaka Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) kujipanga kikamilifu katika maandalizi ya mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027, hususan katika kuhakikisha wageni watakaofika nchini wanapata huduma bora za matibabu bila vikwazo.

Agizo hilo limetolewa l na Naibu Waziri wa Afya Mhe. Dkt. Florence Samizi (Mb.) ambaye amesema NHIF ina jukumu muhimu la kuratibu suala la bima ya afya wakati wa mashindano hayo ili kuhakikisha wageni wanapata huduma za matibabu kwa urahisi pindi wanapohitaji huduma hizo.

“Tuwape uhakika wa huduma bora ili waone fahari kuwapo hapa nchini katika kipindi chote cha mashindano hayo,” amesema Dkt. Samizi.

Amesema maandalizi ya huduma za matibabu yanapaswa kuzingatia pia huduma za dharura pamoja na huduma maalum, ikiwemo za moyo na mifupa, ili kukidhi mahitaji mbalimbali ya afya yatakayoweza kujitokeza wakati wa mashindano.

Aidha alidokeza kuwa tayari Wataalamu kutoka Shirikisho la Soka Afrika (CAF) wamekagua Vituo vya kutolea huduma kwa alengo la kujiridhisha na wamefurahishwa na utayari unaoonyeshwa katika maandalizi ya huduma za matibabu jambo linaloonesha kuwa Tanzania inajiandaa kuhakikisha AFCON 2027 inafanyika katika mazingira salama na yenye huduma bora.

Ameitaka NHIF kushirikiana kwa karibu na Wizara ya Afya, vituo vya kutolea huduma na wadau wengine kuhakikisha mfumo wa huduma za matibabu wakati wa mashindano hayo unakuwa imara, unaopatikana kwa wakati na unaokidhi viwango vinavyohitajika.

Akizungumzia hilo Mkurugenzi Mkuu waa NHIF, Dkt. Irene Isaka alisema kuwa tayari Mfuko umeshajipanga na umeandaa kifurushi maalumu kwa ajili ya wageni wote watakaokuja nchini kwa ajili ya mashindano hayo.

“Tayari tumejipanga na tuna kifurushi ambacho tutakileta Wizarani ili tupate baraka ya Wizara hivyo tunashukuru sana kwa maelekezo haya ambayo yanaboresha na kuhakikisha tunajipanga vyema,” alisema Dkt. Isaka. ‎


‎ ‎ ‎NAIBU Waziri wa Afya, Mhe Dkt. Florence George Samizi (Mb), amelipongeza Baraza la Wafanyakazi la Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) kwa kuwa moja ya mabaraza bora nchini. Amelitaka baraza kuhakikisha ajenda ya Bima ya Afya kwa wote inawafikia wananchi wengi zaidi.

Nimefurahi kusikia kwamba katika kipindi cha mwaka wa fedha 2025/2026 Mfuko umeweza kufikia 10.7% ya Wananchi toka 8% ya wananchi iliyodumu kwa takriban miaka 10. Pamoja na pongezi hizo Mh. NAIBU WAZIRI ameutaka Mfuko kutumia TEHAMA na kusajili wanachama wengi zaidi ili kutimiza ahadi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwafikishia wananchi wote huduma za bima ya afya. Hii itasaidia wananchi kuondokana na umaskini pale wanapopata maradhi. ‎

 ‎Dkt. Samizi ametoa maelekezo Hayo wakati wa mkutano wa nne wa wa Baraza la 4 wafanyakazi NHIF, Jijini Arusha, na kusisistiza menejimenti ya wafanyakazi wa NHIF kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia uadilifu, weledi na uwajibikaji, huku wakisikiliza na kutatua kwa wakati kero za wananchi. 

‎ ‎Aidha, amesisitiza umuhimu wa kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kuwa na bima ya afya. Kutoa huduma bora na kuwa na mfumo wa kupokea mrejesho toka kwa wananchi. ‎ ‎Katika kuelekea maadhimisho ya miaka 25 tangu kuanzishwa kwa NHIF, Dkt. Samizi amesema ni muhimu mfuko huo kuonesha mafanikio yaliyopatikana. 

Kuwepo kwa NHIF kumesaidia kuboresha huduma za Afya kwa kulipa madai na kutoa mikopo kwa vituo vya afya. Ni vema wanachi wakajulishwa hatua kubwa iliyofikiwa katika huduma za Afya na mchango wa NHIFkatika Sekta hii muhimu. 

Mlianza na vituo vichache sana mwaka 2001 hivi sasa yaani mwaka wa Fedha 2025/26 mmesajili zaidi ya vituo 10,600 nchi nzima. Ni vema kuonesha namna mlivyokabiliana na changamoto za wakati ule na namna zilivyowasaidia kuboresha Mfuko katika utoaji wa huduma. ‎ 

‎Amesema mafanikio hayo yanadhihirishwa na kujituma, ushirikiano, umoja na mshikamano miongoni mwa watumishi wa NHIF ili kufikia malengo ya mfuko kwa lengo la kutekeleza jitihada za Serikali za kuhakikisha wananchi wanapata bima ya Afya. ‎

 ‎Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, Dkt. Irene Isaka, ameeleza mafanikio yaliyopatikana ikiwa ni pamoja na kupunguza muda wa kilipa madai toka zaidi ya siku 90 hadi wastan wa siku 50 kwa mwaka wa Fedha 2025/2026. Vile vile alieleza kwamba Mfuko umeendelea kuimarika ambapo ziada imeongezeka kwa 57% Mfuko umepunguza matumizi kwa asilimia13% na uwekezaji umeongezeka kwa 106%.

Hii imewezesha Mfuko kuendeleza kifurushi cha wanafunzi, Toto Afya. Mfuko kusajili kifurushi cha tarangire, Mikumi, Ngorongoro, Serengeti Tanzanite na kifurushi cha vikundi yaani Umoja Afya ambacho ni sh. 60, 000 kwa matibabu ya mwaka mzima.

Vile vile alielezea mikakati inayotekelezwa na mfuko huo katika kufikia malengo yake ikiwa ni pamoja na matumizi ya TEHAMA kwenye usajili, uchakataji madai na kupambana na udanganyifu.

 Mfuko pia unashirikisha Sekta Binafsi katika usajili wa wanachama na katika huduma za matibabu. ‎ ‎Mwakilishi wa chama Cha wafanyakazi TUGHE, Bw.Paul wamepongeza baraza Hilo kuzingati misingi ya Kazi stahiki za wafanyakazi kwenye taasisi hiyo. ‎

 ‎Baadhi ya wafanyakazi walioshiriki semina elekezi ya siku mbili wamesema wamepata maarifa na mwelekeo mpya ambao utawasaidia kuboresha utendaji wao wa kazi na utoaji wa huduma kwa wananchi.

‎ Bima ya Afya kwa wote! Jiunge sasa!
Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Ndg. Abdi Mahmoud Abdi, amesema uwepo wa maskani za vijana wa CCM ni miongoni mwa njia muhimu za kuimarisha umoja na mshikamano miongoni mwa wanachama na viongozi wa chama katika ngazi mbalimbali.

Ndg. Abdi ameyasema hayo wakati wa ufunguzi wa Maskani ya CCM ya Kibweni Shaba Juu, iliyopo katika Jimbo la Mkwajuni, Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Amesema maskani zina nafasi muhimu katika kuwakutanisha wanachama, hususan vijana, na kuwawezesha kubadilishana mawazo, kujenga na kuimarisha mahusiano, pamoja na kushirikiana katika shughuli mbalimbali za maendeleo na za chama.

Aidha, Ndg. Abdi amewataka wana-CCM na wanamaskani kuendelea kudumisha umoja na mshikamano uliopo nchini, sambamba na kuunga mkono juhudi zinazofanywa na viongozi wakuu wa nchi na chama katika kuwaletea wananchi maendeleo.

Amesisitiza kuwa umoja, mshikamano na ushirikiano ni msingi muhimu katika kuendelea kuijenga CCM imara, yenye uwezo wa kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kwa manufaa ya wananchi.










Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Ndg. Abdi Mahamoud Abdi, amewatembelea na kuwajulia hali wazee wa chama, akiwemo Balozi wa CCM wa Shina Namba 21, Ndg. Mtumwa Ali Ndevu, nyumbani kwake Mkwajuni, Zanzibar.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Ndg. Abdi amesema ni muhimu kwa viongozi na wanachama wa CCM kuendelea kuwathamini, kuwaheshimu na kuwajali wazee ambao wamekuwa sehemu muhimu ya historia, ujenzi na mafanikio ya Chama Cha Mapinduzi.

Amesema CCM inatambua mchango mkubwa wa wazee wake katika kulinda misingi, misimamo na maadili ya chama, hivyo viongozi na wanachama wana wajibu wa kuendelea kuwa karibu nao na kujifunza kutokana na uzoefu wao.

Kwa upande wake, Ndg. Mtumwa Ali Ndevu amemshukuru Ndg. Abdi kwa kumtembelea na kumjulia hali, akisema kitendo hicho ni ishara ya upendo, heshima na mshikamano uliopo ndani ya Chama Cha Mapinduzi.

Ziara hiyo ni sehemu ya juhudi za viongozi wa CCM Zanzibar kuendelea kuwa karibu na wanachama, viongozi wastaafu na wazee wa chama, kwa lengo la kuimarisha mshikamano, kuhifadhi historia ya chama na kuendeleza misingi ya Chama Cha Mapinduzi.



Na Said Mwishehe,Michuzi TV HALMASHAURI ya Jiji la Dar es Salaam imesema viongozi wakuu wa kitaifa wameweka msisitizo wa kuhakikisha Jiji hilo linakuwa safi wakati wote, hivyo Jiji hilo limewahimiza wananchi kuwa sehemu ya juhudi hizo kuhakikisha mazingira yanakuwa safi.

Akizungumza leo Septemba 5,2026 wakati akishiriki usafi katika soko la Buguruni, Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam Elihuruma Mabelya amesema pia ushiriki wa wananchi katika zoezi la usafi umeendelea kuimarika, huku viongozi kutoka ngazi mbalimbali nao wakishiriki katika utekelezaji wa zoezi hilo.

Amesema usafi wa mazingira jijini humo hufanyika kwa ushirikiano wa viongozi na wananchi, ambapo zoezi la usafi hufanyika kila Jumamosi pamoja na kuendelea kuhamasisha usafi katika siku nyingine za wiki.

Mkurugenzi huyo amesema utekelezaji huo unaendana na maelekezo, sera na mwelekeo wa Serikali ya Awamu ya Sita wa kuhakikisha kila mmoja anakuwa sehemu ya usafi na kujenga utamaduni wa kushirikiana katika kulinda mazingira.

Amesema Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam inaendelea kusimamia Dira ya Maendeleo ya Taifa pamoja na Sera ya Taifa ya Mazingira kwa kuhakikisha mipango ya usafi na utunzaji wa mazingira inatekelezwa ipasavyo.

Katika hatua nyingine, amesema Jiji linaelekea katika mwelekeo mpya wa usimamizi wa taka, ikiwemo ukusanyaji, usafirishaji na utupaji wa taka, huku sekta binafsi ikitarajiwa kushirikishwa zaidi kuongeza nguvu katika juhudi za kulifanya Dar es Salaam kuwa safi.

Ametoa wito kwa wananchi katika kata zote za Jiji hilo pamoja na viongozi ndani ya Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kuwa sehemu muhimu ya kuhakikisha mazingira ya jiji yanakuwa safi wakati wote.

Amesema maeneo yanayopaswa kupewa kipaumbele katika suala la usafi ni pamoja na mitaro, barabara, masoko, miundombinu ya umma na maeneo ya makazi ya wananchi.

Kuhusu wafanyabiashara wanaofanya biashara katika maeneo yasiyo rasmi, Mkurugenzi huyo amesema Halmashauri inaendelea kutekeleza utaratibu maalumu wa kuhakikisha wafanyabiashara hao wanahamishiwa katika maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya biashara.

Amesema baadhi ya wafanyabiashara wamekuwa wakipanga biashara zao kandokando ya barabara na kusababisha msongamano, hali ambayo amesema si salama na haiendani na mipango ya matumizi bora ya maeneo ya jiji.

Amesema katika zoezi lililofanyika eneo la Soko la Buguruni, baadhi ya wafanyabiashara waliokuwa wamepanga biashara zao nje ya soko wameelekezwa na kurejea ndani ya soko baada ya kutambua kuwa eneo walilokuwa wakifanyia biashara halikuwa sahihi.

Mkurugenzi huyo amesema mpango wa kuwapanga wafanyabiashara unaendelea, huku Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam ikitenga Shilingi bilioni 6.7 katika mwaka wa fedha kwa ajili ya ujenzi, ukarabati na uzalishaji wa masoko.

Amesema lengo la mpango huo ni kuhakikisha wafanyabiashara wanaofanya shughuli zao katika maeneo yasiyo rasmi wanapata maeneo sahihi ya kufanyia biashara kupitia masoko yanayojengwa na kukarabatiwa na Halmashauri.

Aidha, amesema kwa ridhaa na baraka za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, mpango wa ujenzi wa soko la kisasa eneo la Jangwani, maarufu kama Figo Sambusa, unaendelea kwa ajili ya kuwahudumia machinga na wafanyabiashara wadogo.

Amesema soko hilo linatarajiwa kuwa na uwezo wa kuchukua wafanyabiashara zaidi ya 80, hatua ambayo amesema inaonyesha dhamira ya Serikali ya kuwawezesha wafanyabiashara wadogo kupata maeneo rasmi ya biashara, kujikwamua kiuchumi na kuwa sehemu muhimu ya kuchangia katika pato la Taifa.




 

Na Janeth Raphael - MichuziTv

WAZIRI wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, ameitaka Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) kuimarisha mfumo wa udahili na usajili wa wanafunzi wa elimu ya juu ili kuhakikisha vyuo havipokei wanafunzi zaidi ya uwezo wa miundombinu na wakufunzi waliopo.

Prof. Mkenda amesema hatua hiyo ni muhimu katika kulinda ubora wa elimu ya juu nchini, huku ikihakikisha wanafunzi wanapata nafasi za masomo kwa haki, uwazi na kwa kuzingatia uwezo halisi wa kila chuo.

Waziri huyo ameyasema hayo leo, Septemba 5, 2026, jijini Dodoma, baada ya kukutana na Makamu Wakuu wa Vyuo Vikuu pamoja na Wenyeviti wa Mabaraza ya vyuo vikuu nchini katika kikao kilichojadili masuala mbalimbali yanayohusu sekta ya elimu ya juu, ikiwemo udahili na usajili wa wanafunzi.

Amesema Serikali inalenga kuhakikisha mfumo wa udahili unakuwa bora na wenye ufanisi, ili kuepusha changamoto zinazoweza kujitokeza pale vyuo vinapodahili wanafunzi wengi kuliko uwezo wa kuwahudumia.

“Tumefanya hivyo kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunatengeneza mfumo mzuri ambao hautaleta utata, hautakuwa na kuweka idadi ya wanafunzi kuliko uwezo wa kufundisha,” amesema Prof. Mkenda.

Prof. Mkenda amewataka wanafunzi wanaotarajia kujiunga na vyuo vikuu kuendelea kufanya maombi yao wakati wakisubiri maelekezo zaidi kutoka TCU kuhusu utaratibu wa udahili.

Amesema mfumo unaoandaliwa unalenga kuweka uwiano kati ya ongezeko la mahitaji ya elimu ya juu na uwezo wa vyuo kutoa elimu bora, huku maslahi ya wanafunzi yakilindwa.

Serikali kuongeza nafasi za elimu ya juu

Waziri Mkenda amesema Serikali inaendelea kuongeza uwezo wa vyuo vikuu nchini kupitia ujenzi na upanuzi wa kampasi katika mikoa mbalimbali ili kuongeza nafasi za wanafunzi kupata elimu ya juu.

Amesema uwekezaji huo utawezesha vijana wengi zaidi kupata fursa za masomo bila kulazimisha vyuo kupokea idadi kubwa ya wanafunzi ambayo inaweza kuathiri ubora wa elimu.

Kwa mujibu wa Prof. Mkenda, Tanzania bado haijafikia kiwango cha uandikishaji wa wanafunzi katika elimu ya juu kinacholengwa, hivyo Serikali itaendelea kuongeza nafasi za masomo sambamba na kuhakikisha viwango vya elimu vinadumishwa.

Amesema lengo ni kujenga mfumo wa elimu ya juu unaotoa fursa kwa vijana wengi zaidi na wakati huo huo kuwaandaa kwa ufanisi ili waweze kukidhi mahitaji ya soko la ajira




TCU YAWEKA MKAZO KWENYE UDAHILI WA 2026/2027

Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa TCU, Prof. Charles Kihampa, amesema kikao hicho kimejadili kwa kina masuala ya udahili wa wanafunzi, ubora wa elimu pamoja na hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali katika kuendeleza sekta ya elimu ya juu.

Amesema TCU, Serikali na vyuo vikuu wamekubaliana kuendelea kushirikiana katika kuboresha mifumo ya udahili kwa kuzingatia mabadiliko na mahitaji yanayoendelea katika sekta ya elimu.

Prof. Kihampa amesema ongezeko linalotarajiwa la wanafunzi kutokana na mabadiliko mbalimbali ya sera linahitaji maandalizi ya mapema kutoka kwa Serikali, TCU na vyuo vikuu ili kuhakikisha uwezo wa kutoa elimu unaendana na idadi ya wanafunzi wanaotarajiwa.

Naye Mwenyekiti wa Baraza la Chuo Kikuu cha Teolojia cha Lweru, Aggrey Mlimuka, amesisitiza umuhimu wa vyuo vikuu kusimamia ubora wa elimu na kuhakikisha wahitimu wanakuwa na maarifa, uwezo na weledi unaokidhi mahitaji ya soko la ajira.

Amesema kila chuo kina wajibu wa kuhakikisha programu zake zinazalisha wataalamu wenye uwezo, akibainisha kuwa endapo ubora hautasimamiwa, soko la ajira litawachuja wahitimu kwa kuzingatia uwezo wao.

DIRISHA LA PILI LA UDAHIL KUFUNGULIWA WIKI IJAYO

Awali, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Ushirika Moshi (MoCU), Prof. Alfred Sife, amesema vyuo vikuu vimekubaliana kuendelea kuboresha mchakato wa udahili kwa mwaka wa masomo 2026/2027 ili kuhakikisha wanafunzi wanaodahiliwa wanakidhi vigezo na wanajiunga na programu zinazolingana na sifa zao.

Prof. Sife amesema moja ya hoja kubwa iliyojadiliwa katika kikao hicho ni mwenendo wa udahili unaoendelea, ambapo dirisha la kwanza la maombi limekamilika na dirisha la pili linatarajiwa kufunguliwa wiki ijayo.

Amesema kuimarishwa kwa mfumo huo kutasaidia kuhakikisha wanafunzi wenye sifa wanapata nafasi katika programu na vyuo vinavyowafaa, huku taratibu, kanuni na sheria za udahili zikizingatiwa.

Ameongeza kuwa ushirikiano kati ya Serikali, TCU na vyuo vikuu ni muhimu katika kuboresha mifumo ya elimu na kuhakikisha uwekezaji unaofanywa katika sekta hiyo unazalisha wahitimu wenye uwezo wa kukidhi mahitaji ya taifa na soko la ajira.



▪️︎ Aelekeza fedha zinazookolewa kwenye kubana matumizi zielekezwe kwenye huduma za wananchi

▪️︎ Aagiza magari ya kubeba wagonjwa yawe na mafuta, aonya wanaowachangisha wagonjwa

▪️︎ Ampongeza Afisa Elimu aliyesimamia shule kuongoza kitaifa


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali imejipanga kufanya mageuzi makubwa katika sekta ya elimu, ikiwemo kuhakikisha kila kijiji kinakuwa na shule ya sekondari, na zaidi ya vyumba 16,000 vya madarasa vikitarajiwa kujengwa ili kukidhi ongezeko la wanafunzi.

Dkt. Mwigulu amesema hayo leo, Jumamosi, Septemba 05, 2026, wakati akizungumza na wananchi wa Wilaya ya Bahi, mkoani Dodoma, katika Viwanja vya Halmashauri ya Bahi, alipokuwa katika ziara ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo, kuwasikiliza wananchi na kushughulikia changamoto zinazowakabili.

Amesema uamuzi wa kuongeza muda wa elimu ya lazima hadi kidato cha nne unaleta mahitaji makubwa ya miundombinu ya elimu, yakiwemo madarasa, maabara na maktaba.

“Tunaposema elimu ya lazima itakuwa mpaka kidato cha nne, maana yake tunasema kila kijiji kiwe na sekondari. Tunaongelea mahitaji ya madarasa zaidi ya vyumba 16,000.”

Waziri Mkuu amesema Serikali haitaki kuona watoto wakirejea katika mazingira ya kusoma chini ya miti, kukosa madarasa au kusoma katika mazingira ya msongamano, akisisitiza kuwa maandalizi ya mapema ni muhimu kukabiliana na mahitaji hayo.

Amesema Serikali pia inahitaji kuongeza idadi ya maabara, akieleza kuwa mahitaji yanaweza kufikia takribani maabara 8,000, pamoja na maktaba, ili kuimarisha mazingira ya kujifunzia na kufundishia.

Aidha, Dkt. Mwigulu amewataka viongozi wa Serikali kubadili baadhi ya taratibu zinazoweza kuokoa fedha na kuelekeza rasilimali hizo kwenye huduma zinazogusa maisha ya wananchi moja kwa moja.

Amesema viongozi wanapaswa kuweka mbele wajibu wa kuleta maendeleo kuliko kutafuta sifa zinazohusisha gharama zisizo za lazima.

Ametoa mfano wa misafara mikubwa ya viongozi na mikutano inayohusisha idadi kubwa ya watendaji kusafiri kwenda vituo vingine, akisema fedha zinazoweza kuokolewa zinapaswa kuelekezwa katika ujenzi wa madarasa, maabara, madawati na huduma nyingine muhimu.

“Kila tunapoweza kupata akiba tuielekeze kwenye jambo linalogusa maisha ya wananchi wetu ya kila siku.”

Kuhusu huduma za afya, Waziri Mkuu amewataka viongozi kuhakikisha magari ya kubeba wagonjwa ya Serikali yanakuwa na mafuta na wagonjwa wanaohitaji rufaa hawalazimishwi kuchangisha fedha kwa ajili ya mafuta.

Amesema Serikali imewekeza kwa kiasi kikubwa katika ujenzi wa hospitali, vituo vya afya, ununuzi wa magari ya kubeba wagonjwa, vifaa tiba na ajira za wataalamu, hivyo watendaji wanapaswa kuhakikisha uwekezaji huo unawanufaisha wananchi.

Ameonya kuwa mtumishi anayemlazimisha mgonjwa au ndugu yake kuchangisha fedha kwa ajili ya mafuta ya gari la kubeba wagonjwa anapaswa kuchukuliwa hatua, huku akiwataka wananchi kuripoti watumishi wanaokiuka taratibu na kuwanyima wananchi huduma wanazostahili.

Dkt. Mwigulu pia amempongeza Mkuu wa Divisheni ya Elimu ya Awali na Msingi, Boniface Wilson Mwakasole, kwa utendaji wake katika kuboresha elimu wilayani Bahi, akieleza kuwa amefuatilia kazi yake na kubaini mafanikio yaliyopatikana, ikiwemo Shule ya Msingi Chiona kuongoza kitaifa katika elimu ya msingi.

Amesema watendaji wanaofanya vizuri wanapaswa kutambuliwa na kupewa majukumu makubwa zaidi yanayolingana na uwezo wao.

Akimtolea mfano Boniface Wilson Mwakasole, Waziri Mkuu ameelekeza kuwa endapo mtendaji huyo ataondolewa Bahi, apandishwe cheo na kupewa jukumu kubwa zaidi kutokana na utendaji wake.

“Huyo mtu mzuri wa aina hiyo kama mnataka kumhamisha, mpandisheni; mpeni mkoa kama mnataka kumtoa Bahi. Kama hamjapata mkoa, msimhamishe, mbakizeni hapa hapa. Amefanya kazi nzuri ya kuigwa.”

Amesema utendaji mzuri unapaswa kuwa msingi wa kumpa mtumishi majukumu makubwa, akisisitiza kuwa mtu anayefanya kazi vizuri hahitaji kuomba nafasi kwa kutumia ushawishi kwa sababu kazi yake yenyewe inamtambulisha.“Mtu anayefanya kazi nzuri wala hahitaji lobbying, hauhitaji kuomba-omba kazi; kazi inakutambulisha.”

Amesema Serikali inapaswa kuwa na utamaduni wa kutambua na kupongeza watendaji wanaofanya vizuri, sambamba na kuchukua hatua kwa wale wanaoshindwa kutimiza wajibu wao.

Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kutekeleza miradi ya maendeleo katika Wilaya ya Bahi, ikiwemo miradi ya maji, afya, elimu, umwagiliaji, barabara na madaraja.

Amesema amepokea mahitaji mbalimbali yaliyowasilishwa na viongozi wa wilaya na mkoa na amemtaka Naibu Waziri anayesimamia Serikali za Mitaa kuyafuatilia kwa karibu ili hatua zichukuliwe katika maeneo yenye uhitaji.

Pia ameeleza kuwa maeneo yanayounganisha miji na vijiji, lakini wananchi wake bado wanaishi katika mazingira ya vijijini, yataendelea kunufaika na utaratibu wa kuunganishiwa umeme kwa gharama zinazotumika maeneo ya vijijini.









Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Dkt. Mahmoud Thabit Kombo (Mb), amekutana na kuagana na Balozi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Mheshimiwa Jean Pierre Massala, ambaye amehitimisha muda wake wa uwakilishi hapa nchini.

Mhe. Kombo alikutana na Balozi huyo Septemba 4, 2026, katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.

Katika kikao hicho, Waziri Kombo alimpongeza Balozi Massala kwa mchango wake katika kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na ushirikiano wa pande mbili kati ya Tanzania na DRC, hususan katika maeneo ya maendeleo, biashara na uwekezaji.

Waziri Kombo alisema Tanzania imeazimia kuimarisha zaidi ushirikiano wa kimkakati na DRC katika sekta mbalimbali, zikiwemo uchukuzi, madini, mafuta na gesi, ulinzi na usalama, pamoja na kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya pamoja yenye manufaa kwa wananchi wa nchi hizo mbili.

Miongoni mwa miradi ya kipaumbele ni ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR), inayolenga kuunganisha Tanzania na DRC kupitia Burundi, pamoja na ujenzi wa Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano ya Mawimbi ya Mwanga kutoka Kigoma nchini Tanzania hadi Kalemie, Mkoa wa Tanganyika nchini DRC, kupitia Ziwa Tanganyika.

Aidha, Tanzania na DRC zimekubaliana kuharakisha uanzishwaji wa Tume ya Pamoja ya Kiuchumi (JEC), ambayo inalenga kurahisisha utekelezaji wa miradi ya pamoja na kutengeneza fursa mpya za kiuchumi kwa nchi hizo.

Kwa upande wake, Balozi Massala ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa ushirikiano alioupata katika kipindi chake cha uwakilishi nchini na kusisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano wa kimkakati katika sekta mbalimbali za maendeleo kati ya Tanzania na DRC.















Top News