Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni baada ya kuwasili katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 06 Agosti, 2026.
 Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta akisaini Kitabu cha wageni, baada ya kuwasili katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 06 Agosti, 2026. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akimpigia makofi Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni baada ya kusaini Kitabu cha wageni katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 06 Agosti, 2026.

 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni baada ya kuwasili katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 06 Agosti, 2026.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni baada ya kuwasili katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 06 Agosti, 2026.
 Waziri wa Nishati wa Tanzania Mhe. Deogratius Ndejembi akizungumza kwenye mkutano wa Waandishi wa Habari baada ya hafla ya utiaji saini Hati ya Makubaliano kuhusu mapendekezo ya kuendeleza Tanga kama Kituo cha Nishati cha Kikanda ulioshuhudiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni, Ikulu, jijini Dar es Salaam, tarehe 06 Agosti, 2026.
 Waziri wa Nishati na Maendeleo ya Madini Mhe. Dkt. Musenero Masanza wa Uganda akizungumza kwenye mkutano wa Waandishi wa Habari baada ya hafla ya utiaji saini Hati ya Makubaliano kuhusu mapendekezo ya kuendeleza Tanga kama Kituo cha Nishati cha Kikanda ulioshuhudiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni, Ikulu, jijini Dar es Salaam,
tarehe 06 Agosti, 2026.





Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akutana na Kuzungumza na Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni, Ikulu Jijini Dare es Salaam.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni wakishuhudia utiaji saini Hati ya Makubaliano kuhusu mapendekezo ya kuendeleza Tanga kama Kituo cha Nishati cha Kikanda katika viwanja vya Ikulu, jijini Dar es Salaam, tarehe 06 Agosti, 2026. Hati hiyo ya Makubaliano imesainiwa kati ya Shirika la Maendeleo la Petroli Tanzania (TPDC) chini ya Mkurugenzi Mtendaji Bw. Mussa Makame, Kampuni ya Taifa ya Mafuta ya Uganda (UNOC) chini ya Mkurugenzi Mtendaji Bi. Proscovia Nabbanja pamoja na Kampuni ya Biashara ya Mafuta na Nishati ya Vitol ya Bahrain, chini ya Mkurugenzi Mtendaji wake Tom Baker.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni wakishuhudia utiaji saini Hati ya Makubaliano kuhusu mapendekezo ya kuendeleza Tanga kama Kituo cha Nishati cha Kikanda katika viwanja vya Ikulu, jijini Dar es Salaam, tarehe 06 Agosti, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiagana na Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni mara baada ya kuhitimisha ziara rasmi ambapo walishuhudia utiaji saini Hati ya Makubaliano kuhusu mapendekezo ya kuendeleza Tanga kama Kituo cha Nishati cha Kikanda kuwasili katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 06 Agosti, 2026.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Gerald Mweli, amewapongeza Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) kwa mchango wake mkubwa katika utoaji wa huduma za ujenzi na usimamizi wa majengo ya Serikali, akieleza kuwa taasisi hiyo imekuwa mshirika muhimu katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya wizara.

Mweli ameyasema hayo Agosti 6, 2026, baada ya kutembelea banda la TBA katika Maonesho ya Kilimo Nanenane Kitaifa yanayoendelea jijini Dodoma, amesema Wizara ya Kilimo imefanya kazi nyingi kwa kushirikiana na TBA, ikiwemo usimamizi wa ujenzi wa maghala, usanifu wa jengo la wizara pamoja na usimamizi wa miradi hiyo kwa weledi na ubora wa hali ya juu.

Ameeleza kuwa TBA imeendelea kujidhihirisha kama taasisi yenye uwezo wa kutoa huduma za ujenzi na usimamizi wa majengo zinazokidhi viwango, si kwa taasisi za serikali pekee bali pia kwa sekta binafsi, jambo linalochangia kuimarisha miundombinu ya maendeleo nchini.

Mweli amewahimiza wananchi na wadau wanaotembelea Maonesho ya Nanenane kuhakikisha wanapita katika banda la TBA lililopo eneo la Private Sector Pavilion, ili kujionea huduma mbalimbali zinazotolewa na wakala huo pamoja na kupata taarifa kuhusu fursa zilizopo katika sekta ya ujenzi na usimamizi wa majengo.




Na Janeth Raphael -MichuziTv

Katika hatua ya kuimarisha ubora wa elimu nchini, Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM) umetangaza kuimarisha na kupanua mafunzo yanayolenga kuwajengea uwezo viongozi wa sekta ya elimu ili kuongeza ufanisi katika usimamizi wa shule na taasisi za elimu.

Akizungumza na waandishi wa habari Agosti 6, 2026, jijini Dodoma, Mtendaji Mkuu wa ADEM, Dkt. Maulid Maulid, amesema taasisi hiyo inaendelea kutekeleza mkakati wa kuwapa viongozi wa elimu maarifa na ujuzi wa kisasa unaowawezesha kukidhi mahitaji ya sekta ya elimu inayobadilika kwa kasi.

Amesema mafunzo hayo yanawahusisha wakuu wa shule, walimu wakuu, maafisa elimu wa kata, halmashauri na mikoa, pamoja na wathibiti ubora wa shule, kwa lengo la kuongeza uwajibikaji, kuimarisha utawala bora na kuboresha usimamizi wa rasilimali za elimu.

Kwa mujibu wa Dkt. Maulid, tangu kuanzishwa kwa programu ya Stashahada ya Uongozi, Usimamizi na Utawala katika Elimu (DELMA), wahitimu 8,599 wamehitimu kati ya mwaka 2002 na 2025. Aidha, wahitimu 2,263 wamekamilisha Stashahada ya Uthibiti Ubora wa Shule (DSQA) tangu mwaka 2016.

Katika mwaka wa masomo 2025/2026 pekee, ADEM ilidahili wanafunzi 2,016, huku wengi wao wakijiunga na programu ya DELMA, hatua inayoonesha kuongezeka kwa mahitaji ya mafunzo ya uongozi wa elimu nchini.

Dkt. Maulid amesema mafunzo hayo yamekuwa na mchango mkubwa katika kuboresha utendaji wa viongozi wa elimu, kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika usimamizi wa shule na kuongeza uwajibikaji katika utoaji wa huduma za elimu.

Ameeleza kuwa kupitia Mradi wa Kuimarisha Ufundishaji na Ujifunzaji kwa Shule za Awali na Msingi (BOOST), ADEM imepokea zaidi ya shilingi bilioni 16 kwa ajili ya kutoa mafunzo ya uongozi kwa viongozi wa elimu katika kipindi cha miaka mitano.

Kupitia mradi huo, zaidi ya walimu wakuu 17,817, waratibu elimu wa kata zaidi ya 3,900 pamoja na maafisa elimu wa wilaya na mikoa tayari wamenufaika na mafunzo hayo, yanayolenga kuboresha huduma za elimu katika shule za umma.

Mbali na mafunzo, ADEM inaendelea kufanya tafiti na kutoa ushauri wa kitaalamu kuhusu maboresho ya sera za elimu, huku ikipanua ushirikiano na taasisi za ndani na nje ya nchi ili kuimarisha matumizi ya teknolojia na ubora wa mafunzo.

Kwa mwaka wa fedha 2026/2027, ADEM imejipangia kuongeza udahili wa wanafunzi wa mafunzo ya muda mrefu hadi 3,500, kuanzisha programu mpya za mafunzo, kuboresha miundombinu ya kampasi zake za Bagamoyo, Mbeya na Mwanza pamoja na kupanua matumizi ya TEHAMA.

Hatua hizo zinatarajiwa kuongeza uwezo wa viongozi wa elimu kusimamia mageuzi ya sekta hiyo na kuchochea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, inayolenga kujenga mfumo wa elimu wenye ushindani na unaokidhi mahitaji ya maendeleo ya taifa.







Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Dkt. Charles Msonde, ameupongeza Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA) kwa maboresho makubwa ya utoaji wa huduma, hususan matumizi ya teknolojia yanayorahisisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi.

Dkt. Msonde amesema hayo leo, Agosti 5, 2026, alipotembelea banda la TEMESA katika Maonesho ya 33 ya Kitaifa ya Kilimo (Nane Nane 2026) yanayoendelea katika Viwanja vya Nzuguni, jijini Dodoma.



Dkt.Msonde Amesema kuwa ameridhishwa na maendeleo makubwa yaliyofikiwa na TEMESA, akieleza kuwa uimarishaji wa huduma za kidijitali pamoja na ongezeko la ubora wa mafundi umeongeza ufanisi wa wakala huo.

“Kilichonifurahisha zaidi ni uimarishaji wa mafundi. Sasa wanafanya kazi kwa weledi mkubwa na wanatengeneza magari kwa ubora. Kwa kweli TEMESA mmenifurahisha sana,hongereni sana” amesema Dkt. Msonde.



Aidha, amesema Serikali na wananchi wanaiamini TEMESA kutokana na mchango wake katika kulinda usalama wa magari ya Serikali na kuhakikisha matumizi sahihi ya fedha za umma. Amewataka viongozi na watumishi wa wakala huo kuendelea kubuni na kuboresha huduma kwa kutumia teknolojia.



Kwa upande wake, Meneja Masoko na Uhusiano kwa Umma- TEMESA, Bi. Martha Joachim, amesema miongoni mwa maboresho yaliyofanywa ni kuhuisha huduma ya ukodishaji wa mitambo kupitia Mfumo wa TIMIS, ambapo wateja sasa wanaweza kuwasilisha maombi ya ukodishaji kwa njia ya kidijitali, hatua iliyopunguza urasimu na muda wa kupata huduma.



Maonesho hayo yenye kauli mbiu “Tambua Soko, Ongeza Tija Kutekeleza Dira 2050”, yanatarajiwa kuadhimishwa tarehe 8 Agosti, 2026.





Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Udhibiti wa Mbegu za Kilimo Tanzania (TOSCI), Nyasebwa E. Chimagu, amesema mbegu za asili ni lazima ziwe na afya na ziwe chini ya utaratibu rasmi wa usimamizi ili kuhakikisha hazina magonjwa na zinaendelea kuhifadhiwa kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Chimagu alitoa kauli hiyo Agosti 5, 2026, jijini Dodoma wakati akizungumza katika mkutano wa wadau wa kilimo ikolojia uliofanyika ndani ya Maonesho ya Kilimo ya Nanenane Kitaifa.

Alisema sheria ya mbegu nchini inaeleza wazi masharti ya usajili, ubora na usimamizi wa mbegu zinazozalishwa kwa ajili ya biashara bila kubagua aina yoyote ya mbegu, Aidha, alibainisha kuwa Tanzania imeanza hatua za awali za kuandaa sheria maalumu kufuatia Mkataba wa Kimataifa wa mwaka 2001, unaolenga kulinda haki za wakulima juu ya mbegu zao za asili pamoja na rasilimali za mimea.

Chimagu alisema nasaba za mimea ni rasilimali muhimu yenye mchango katika maendeleo ya sekta ya kilimo na uchumi wa nchi. Alieleza kuwa kupitia Wizara ya Kilimo na TOSCI, juhudi zimeendelea kufanyika katika kulinda nasaba hizo, huku changamoto kubwa zikitajwa kuwa ongezeko la idadi ya watu na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Alisisitiza kuwa ni muhimu kuhakikisha mbegu za asili zinapatikana kwa wingi ili wakulima wawe na uhuru wa kuchagua aina ya mbegu zinazokidhi mahitaji yao ya uzalishaji.

Kuhusu kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi, Chimagu alisema TOSCI inaendelea kuwekeza katika tafiti za kina zinazolenga kulinda nasaba za mimea na kuboresha mbegu ili ziweze kustahimili mazingira yanayobadilika.

Akitoa mfano, alisema nchini Misri mkulima wa mahindi anaweza kuvuna tani 10 hadi 12 kwa hekta moja kutokana na matumizi ya mbegu bora na teknolojia sahihi, Alisema Tanzania inaendelea kushirikiana na Wizara ya Kilimo kuhakikisha mbegu za asili zinahifadhiwa na kupatikana ili wakulima wawe na uchaguzi wa aina ya mbegu kulingana na mahitaji yao.

Kwa upande wake, Mratibu wa Mtandao wa Mashirika Yanayojishughulisha na Utunzaji wa Bionuai Tanzania (TABIO), Abdullah Ramadhan Mkindi, alisema taasisi hiyo inaendelea kuhamasisha uhifadhi na matumizi ya mbegu za asili pamoja na mifugo ya asili, ikiwemo ng’ombe na kuku wa kienyeji, ili rasilimali hizo zisiendelee kutoweka kutokana na mchango wake katika usalama wa chakula na uhifadhi wa mazingira.

Naye Mratibu wa Utafiti na Masuala ya Kisera kutoka Swiss Aid Tanzania, Gladness Martine, alisema taasisi hiyo imeshiriki mkutano huo kwa lengo la kushirikisha uzoefu kuhusu umuhimu wa tafiti shirikishi zinazowawezesha wakulima kuhifadhi, kulinda na kuendeleza matumizi ya mbegu za asili kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho. 





 Na Janeth Raphael -MichuziTv


Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) limewataka wafugaji nchini kuachana na tabia ya kutumia dawa za mifugo bila ushauri wa wataalamu wa afya ya wanyama, likionya kuwa matumizi yasiyo sahihi ya dawa hizo yanachochea kuongezeka kwa usugu wa vimelea dhidi ya dawa (Antimicrobial Resistance – AMR), tatizo linalotishia afya ya mifugo, binadamu na usalama wa chakula.

Tahadhari hiyo imetolewa na Mratibu wa Mradi wa Kudhibiti Usugu wa Vimelea dhidi ya Dawa (AMR) wa FAO, Elibariki Mwakapeje, wakati akizungumza na wafugaji na wadau wa sekta ya mifugo katika Maonesho ya 31 ya Kilimo ya Nanenane yanayoendelea jijini Dodoma.

Mwakapeje amesema kuwa matumizi ya dawa za mifugo bila ushauri wa wataalamu yameendelea kuwa changamoto inayochangia kupungua kwa uwezo wa dawa kutibu magonjwa mbalimbali ya mifugo, hali inayoweza kusababisha hasara kubwa katika uzalishaji na kuhatarisha afya ya jamii kwa ujumla.

Amefanua kuwa FAO imeamua kutumia jukwaa la Maonesho ya Nanenane kufikisha elimu kwa wafugaji kuhusu matumizi sahihi ya dawa za mifugo, ikiwahamasisha kuhakikisha dawa zinatumika pale tu zinapohitajika na kwa kufuata maelekezo ya wataalamu wa afya ya wanyama.

"Lengo letu ni kuhakikisha wafugaji wanaelewa umuhimu wa kutumia dawa za mifugo kwa usahihi na kutambua madhara makubwa yanayotokana na matumizi holela ya dawa hizo," alisema Mwakapeje.

Amesisitiza kuwa wafugaji wanapaswa kuepuka tabia ya kujinunulia dawa na kuwatibu wanyama bila ushauri wa kitaalamu, akieleza kuwa kufanya hivyo kunaongeza hatari ya kuibuka kwa vimelea vinavyoshindwa kutibika kwa dawa zilizopo.

Kwa mujibu wa Mwakapeje, usugu wa vimelea dhidi ya dawa ni miongoni mwa changamoto kubwa zinazoongezeka duniani, kwani unapunguza ufanisi wa dawa zinazotumika kutibu na kudhibiti magonjwa ya mifugo. Matokeo yake ni kuongezeka kwa gharama za uzalishaji, kupungua kwa tija na kuhatarisha upatikanaji wa chakula salama kwa walaji.

Mbali na matumizi sahihi ya dawa, Mwakapeje aliwahimiza wafugaji kuzingatia kanuni bora za usafi katika ufugaji ikiwemo kusafisha mabanda mara kwa mara, kuhakikisha vyombo vya kunyweshea maji na kulishia mifugo vinakuwa safi pamoja na kuimarisha mazingira ya ufugaji.

Amesema hatua hizo ni muhimu katika kuzuia magonjwa kabla hayajatokea, hivyo kupunguza matumizi yasiyo ya lazima ya dawa za mifugo.


"Afya bora ya mifugo inaanzia kwenye kinga. Wafugaji wanapowekeza katika usafi na biosecurity, wanapunguza kwa kiwango kikubwa uwezekano wa magonjwa na matumizi ya dawa," alieleza.

Aidha, amesema matumizi holela na ya kupita kiasi ya dawa za mifugo yanaweza kuwa na athari zinazovuka sekta ya mifugo pekee, kwani yanaweza kuhatarisha afya ya binadamu kupitia mnyororo wa chakula pamoja na kuathiri mazingira.

Kutokana na hali hiyo, alisisitiza kuwa mapambano dhidi ya usugu wa vimelea yanahitaji ushirikiano wa karibu kati ya wafugaji, madaktari wa mifugo, wataalamu wa afya, taasisi za utafiti, serikali na wadau wote wa mnyororo wa thamani wa chakula.

Mwakapeje amebainisha kuwa FAO itaendelea kutumia majukwaa mbalimbali ya elimu ya umma, ikiwemo Maonesho ya Nanenane, kuongeza uelewa kuhusu matumizi salama na yenye uwajibikaji ya dawa za mifugo ili kulinda afya ya wanyama, afya ya binadamu na kuhakikisha upatikanaji wa chakula salama.

Amehitimisha kwa kuwakumbusha wafugaji kuwa kaulimbiu ya "Kinga ni Bora Kuliko Tiba" ndiyo msingi wa ufugaji wenye tija na endelevu, akisisitiza kuwa kuzuia magonjwa kupitia usafi, lishe bora na usimamizi sahihi wa mifugo ni njia bora zaidi kuliko kutegemea matumizi ya dawa baada ya magonjwa kutokea.



Na Belinda Joseph- Dodoma

Mratibu wa Mtandao wa Mashirika Yanayojishughulisha na Utunzaji wa Bionuai Tanzania (TABIO), Abdallah Ramadhan Mkindi, amesema taasisi hiyo inaendelea kuhamasisha uhifadhi na matumizi ya mbegu za asili pamoja na mifugo ya asili, ikiwemo ng’ombe na kuku wa kienyeji, ili isipotee kutokana na mchango wake mkubwa katika usalama wa chakula na uhifadhi wa mazingira nchini.

Mkindi ameyasema hayo Agosti 5, 2026, jijini Dodoma alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari wakati wa mkutano wa wadau wa kilimo ikolojia uliofanyika katika Maonesho ya Kilimo ya Nanenane Kitaifa.

Amesema mkutano huo umejikita kujadili namna ya kuendelea kutunza mbegu za asili, kuongeza matumizi yake katika uzalishaji wa chakula, pamoja na kuhamasisha mamlaka husika kuzitambua na kuzipa msaada ili ziendelee kukua na kutoa mchango mkubwa katika kuimarisha usalama wa chakula nchini na duniani kwa ujumla.

Aidha, amesema wadau hao wamejadili matumizi ya pembejeo za kilimo hai, ikiwemo viuatilifu vya kudhibiti visumbufu vya mimea na mbolea rafiki kwa mazingira ambazo haziachi mabaki yenye madhara kwa afya ya binadamu baada ya kutumika katika uzalishaji wa mazao.

Mkindi amesema pia wanatambua kuwa wakulima wanahitaji masoko ya uhakika kwa mazao yao, kwa kuwa kilimo ni chanzo kikuu cha kipato na chakula kwa familia nyingi, amesema wakulima wanaozalisha kwa kutumia mbinu za kilimo ikolojia huzalisha mazao mbalimbali, ikiwemo mahindi ya rangi tofauti kama njano, buluu, mekundu na yenye mchanganyiko wa rangi, ambayo yana virutubisho vingi.

Hata hivyo, amesema baadhi ya mamlaka zilizopewa jukumu la kununua nafaka bado hazinunui mahindi hayo kutokana na rangi zake, jambo ambalo linawakosesha wakulima soko licha ya thamani kubwa ya lishe iliyopo kwenye mazao hayo.

Kutokana na hali hiyo, amesema mkutano huo umejadili namna ya kushawishi mamlaka zinazohusika na ununuzi wa mazao kuingiza mahindi hayo katika mfumo rasmi wa ununuzi, sambamba na kuboresha huduma za ugani ili wakulima wapate taarifa sahihi zitakazowawezesha kuongeza tija katika shughuli zao za kilimo.

Kwa upande wake, Mratibu wa Utafiti na Masuala ya Kisera kutoka taasisi ya Swiz Aid Tanzania, Gladness Martine, amesema taasisi hiyo imeshiriki mkutano huo kwa lengo la kushirikisha uzoefu wake kuhusu umuhimu wa tafiti shirikishi katika kuwasaidia wakulima kuhifadhi, kulinda na kuendeleza matumizi ya mbegu za asili kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.






Na Mwandishi Wetu 
CHUO Kikuu cha Dodoma (UDOM), kupitia Mradi wa SAFARI unaotekelezwa kwa ushirikiano na Liverpool School of Tropical Medicine, kimebuni teknolojia ya matumizi ya akili Unde (Artificial Intelligence) inayolenga kusogeza huduma za uchunguzi wa ujauzito (Ultrasound) karibu na wajawazito wanaoishi katika maeneo yenye upungufu wa wataalamu wa afya.

Akizungumza katika Maonesho ya Nanenane yanayoendelea viwanja vya Nzuguni jijini Dodoma, mtafiti wa mradi huo, Hamim Rushoke, amesema mfumo huo unatumia kifaa chenye Kumputa na probe maalumu inayowekwa tumboni kwa mjamzito, ambapo akili unde huchambua taarifa na kutoa majibu ndani ya dakika moja bila kuhitaji mtaalamu wa Ultrasound.

Amesema kifaa hicho kina uwezo wa kubaini umri wa ujauzito, hali ya uhai wa mtoto, mapigo ya moyo, idadi ya watoto waliopo tumboni pamoja na mkao wa mtoto ikiwa ametanguliza kichwa au miguu, kisha kutoa ripoti ambayo inaweza kusomwa na mhudumu yeyote wa afya.

"Teknolojia hii imebuniwa kuondoa changamoto ya ukosefu wa wataalamu wa ultrasound katika zahanati na vituo vya afya. Hata nesi au mkunga akipewa mafunzo ya siku mbili hadi tatu anaweza kuitumia kwa urahisi na kupata majibu sahihi kwa muda mfupi," amesema Rushoke. Ameeleza kuwa lengo kuu la mradi huo ni kuhakikisha wajawazito wa maeneo ya vijijini wanapata huduma za uchunguzi mapema, akibainisha kuwa wanawake wengi hufikia hatua ya kujifungua bila kufanyiwa hata kipimo kimoja cha ultrasound, jambo linaloweza kuhatarisha afya ya mama na mtoto. Kwa mujibu wa Rushoke, kwa sasa mradi huo uko katika hatua ya upembuzi yakinifu ukifanyika chini ya usimamizi wa Wizara ya Afya na Ofisi ya Rais-TAMISEMI, huku ukishirikisha viongozi wa afya, wajawazito na jamii ili kupima namna ambavyo ubunifu huo unapokelewa kabla ya kuidhinishwa kutumika nchini. "Tumepata ushirikiano mkubwa kutoka Wizara ya Afya, TAMISEMI, viongozi wa afya ngazi zote, wahudumu wa afya pamoja na wanawake wajawazito. Dalili zinaonyesha kuwa jamii ipo tayari kuupokea mfumo huu mara baada ya kukamilika kwa utafiti," amesema.

Aidha, amesema mradi huo umezingatia matumizi ya vifaa vya gharama nafuu ikilinganishwa na mashine za kawaida za ultrasound ambazo zinaweza kugharimu zaidi ya Sh milioni 80, wakati mfumo huo unahitaji tablet na probe zenye gharama zisizozidi Sh milioni tano kwa kifaa kizima.

Rushoke amesema mradi huo utaacha vifaa 32 katika zahanati na vituo vya afya 32 vya mkoa wa Dodoma vilivyotumika katika utafiti ili viendelee kutoa huduma bure kwa wananchi, huku akieleza kuwa hatua inayofuata ni Serikali kupanga bajeti ya kusambaza teknolojia hiyo katika maeneo mengine nchin



Na Mwandishi Wetu, Dodoma
MSULUHISHI wa Migogoro ya Bima (TIO) amewataka wakulima waliokata bima za kilimo kupitia benki au mawakala wa bima, kutumia Ofisi ya Msuluhishi wa Migogoro ya Bima pale wanapokumbana na migogoro ya fidia ili kupata haki zao badala ya kukimbilia mahakamani.

Akizungumza katika Maonesho ya Kilimo ya Kimataifa Nanenane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samwel Malecela jijini Dodoma, Msuluhishi Mkuu wa TIO Aloyce Mbunito, alisema ofisi hiyo iliyoanzishwa kwa mujibu wa Sheria Sura ya 394 ina jukumu la kutatua migogoro ya bima kwa njia mbadala ya mahakama.

Alisema ofisi hiyo pia inalenga kulinda watumiaji wa huduma za bima na kuongeza imani ya wananchi katika sekta hiyo.

Mbunito alisema migogoro inayopokelewa mara nyingi inahusisha kukataliwa kwa madai ya fidia, kulipwa fidia isiyolingana na hasara halisi, kucheleweshwa kwa majibu ya madai pamoja na kutokuelewana kuhusu tafsiri ya mikataba ya bima.

Alisema tangu ofisi hiyo ianze kazi mwaka 2025, imefanikiwa kutatua zaidi ya migogoro 2,015, jambo alilosema linaonyesha kuwa wananchi wameanza kutambua umuhimu wa kuitumia kupata haki zao wanapokumbana na changamoto katika huduma za bima.

Aidha, Mbunito alisema katika maonesho hayo wamepokea viongozi wa vyama vya ushirika vya wakulima kutoka mkoani Mara, waliowasilisha changamoto zinazowakabili wakulima wa tumbaku waliopata hasara kutokana na mvua ya mawe, licha ya kuwa walikuwa wamekata bima kupitia benki.

Kwa mujibu wa Mbunito, changamoto kubwa iliyobainika ni baadhi ya wakulima kutofahamu kampuni za bima zilizowahudumia kwa kuwa walikata bima kupitia benki zilizokuwa mawakala wa kampuni hizo.

Alisema pia baadhi ya wakulima hawana mikataba ya bima, ambayo ni nyaraka muhimu katika kufuatilia madai ya fidia pale wanapopata hasara.

Naye Mwenyekiti wa Chama Kikuu cha Ushirika Mara (WAMACU), Momanyi Range, alisema elimu waliyoipata katika banda la Ofisi ya Msuluhishi wa Migogoro ya Bima imewafungua macho kuhusu umuhimu wa kuwa na mikataba ya bima pamoja na kuhifadhi ushahidi wa majanga.

Alisema ushahidi huo unaweza kujumuisha picha za mazao yaliyoharibiwa na majanga, hatua ambayo inaweza kusaidia kurahisisha mchakato wa madai ya fidia.

Range alisema chama hicho sasa kitawaongoza wakulima walioathiriwa kukusanya malalamiko yao, kupata mikataba ya bima kutoka benki husika na kuyawasilisha katika Ofisi ya Msuluhishi wa Migogoro ya Bima ili kuhakikisha wanapata haki zao.

Alisema hatua hiyo itasaidia kuwawezesha wakulima kukabiliana na hasara zinazotokana na majanga na kuendelea na shughuli za uzalishaji bila kuathiriwa zaidi na athari za majanga hayo.


Farida Mangube, Morogoro

Tanzania imepiga hatua katika kuelekea kujitosheleza kwa sukari kufuatia kuanza rasmi kwa uzalishaji katika Kiwanda kipya cha Kisasa cha Sukari Kilombero K4 kilichopo mkoani Morogoro, ambacho kimegharimu zaidi ya shilingi bilioni 700.

Uwekezaji huo unatarajiwa kuongeza uzalishaji wa sukari nchini, kupunguza utegemezi wa uagizaji kutoka nje na kuchochea ukuaji wa uchumi.

Akizungumza katika maonesho ya nanenane Kanda ya Mashariki Mkurugenzi wa Biashara wa Kiwanda cha Sukari Kilombero, Fimbo Butallah, amesema kuanza kwa uzalishaji katika kiwanda hicho kutasaidia kuziba pengo la upungufu wa sukari nchini na kuongeza upatikanaji wa bidhaa hiyo kwa wananchi.

Butallah amesema pia kiwanda hicho kimezingatia tofauti za vipato vya Watanzania kwa kuzalisha sukari katika ujazo wa aina mbalimbali, hatua itakayowezesha wananchi kupata bidhaa hiyo kulingana na uwezo wao wa kifedha.

Kwa upande wake, Meneja wa Ufuatiliaji na Uthibitishaji kutoka Bodi ya Sukari Tanzania, Bahati Hakimu, amesema kukamilika kwa Kiwanda cha Kilombero K4 ni hatua muhimu katika kuongeza uzalishaji wa sukari nchini, huku pia kikitarajiwa kuongeza ajira kwa wakulima wa miwa na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika Bonde la Kilombero.





Na Janeth Raphael -MichuziTv 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametoa wito kwa viongozi wa nchi za Afrika kuharakisha utekelezaji wa miradi ya miundombinu, akisisitiza kuwa maendeleo ya Bara hilo hayatapimwa kwa mipango na sera pekee, bali kwa matokeo yanayoonekana katika maisha ya wananchi.

Rais Samia ameyasema hayo leo jijini Dar es Salaam wakati akifungua Jukwaa la Miundombinu Afrika pamoja na Mkutano Mkuu wa Wanahisa wa Africa50, ambapo alieleza kuwa uwekezaji katika miundombinu ni nguzo muhimu ya kukuza uchumi, kuongeza ushindani wa Afrika, kuvutia wawekezaji na kuimarisha biashara ndani ya bara.

Amesema wananchi wanahitaji kuona matokeo kupitia ujenzi wa barabara bora, reli za kisasa, bandari zenye ufanisi, nishati ya uhakika, maendeleo ya teknolojia pamoja na kuongezeka kwa fursa za ajira.

Akizungumzia hatua zinazochukuliwa na Tanzania, Rais Samia alisema Serikali inaendelea kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kujenga uchumi wa viwanda, jumuishi na unaotegemea ubunifu, ujuzi pamoja na miundombinu ya kisasa.

Amebainisha kuwa Serikali imeendelea kuwekeza katika kuboresha Bandari ya Dar es Salaam, Reli ya Kisasa (SGR), barabara, madaraja na korido za kimkakati ili kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha biashara na usafirishaji katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika.

Rais Samia amesema uwekezaji huo hauwanufaishi Watanzania pekee, bali pia unahudumia nchi jirani zisizo na bandari, zikiwemo Burundi, Rwanda, Uganda, Zambia, Malawi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), hivyo kuimarisha nafasi ya Tanzania kama lango muhimu la biashara na uwekezaji barani Afrika.

Aidha, amesisitiza kuwa Afrika inapaswa kuongeza thamani ya rasilimali zake badala ya kuendelea kusafirisha malighafi, hatua ambayo itaongeza ajira, ujuzi na uwezo wa uzalishaji ndani ya bara.

Katika sekta ya nishati, Rais Samia alieleza kuwa gesi asilia ina nafasi kubwa katika kuimarisha usalama wa nishati, kusaidia ukuaji wa viwanda na kuchochea maendeleo ya uchumi wa Tanzania pamoja na nchi nyingine za Afrika.

Kwa upande wake, Naibu Rais wa Kenya, Prof. Kithure Kindiki, alisema mafanikio ya miradi mikubwa ya miundombinu yanategemea uongozi madhubuti wa kisiasa, sera thabiti na mipango ya muda mrefu.

Prof. Kindiki pia amezitaka nchi za Afrika kuwekeza katika kujenga uwezo wa wataalamu wa ndani, kutumia mifumo bunifu ya kugharamia miradi na kuhakikisha wananchi wanashirikishwa kikamilifu ili wanufaike na maendeleo yanayotekelezwa.

Naye Mwenyekiti wa Africa50 ambaye pia ni Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Dkt. Sidi Ould Tah, alisema taasisi hiyo itaendelea kusaidia nchi za Afrika kubadilisha fursa za miundombinu kuwa miradi inayoweza kufadhiliwa na kutekelezwa kwa ufanisi.

Amesema katika muongo wa pili wa Africa50, kipaumbele kitakuwa kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi, kuhamasisha mitaji na kuimarisha ushirikiano kati ya serikali, taasisi za fedha na sekta binafsi.

Mkutano huo pia ulihusisha mjadala wa mawaziri kutoka Tanzania, Msumbiji, Nigeria na Senegal kuhusu matumizi ya gesi asilia, maendeleo ya viwanda, kuongeza thamani ya rasilimali na ujenzi wa miundombinu ya kikanda.

Katika mjadala huo ilielezwa kuwa zaidi ya Waafrika milioni 600 bado hawana huduma ya umeme, huku Tanzania ikitajwa kuongeza upatikanaji wa nishati safi ya kupikia kutoka asilimia sita mwaka 2021 hadi asilimia 28 mwaka 2026.

Sambamba na mkutano huo, Tanzania ilisaini makubaliano mbalimbali ya ushirikiano yanayolenga kupanua huduma za matibabu ya figo, kuendeleza miradi ya usafirishaji wa umeme kwa ubia wa sekta ya umma na binafsi, pamoja na kuongeza matumizi ya gesi asilia katika shughuli za viwanda.

Makubaliano hayo yanahusisha Africa50, Wizara ya Afya, Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) pamoja na kampuni ya TAQA Arabia.

Akihitimisha hotuba yake, Rais Samia aliipongeza Africa50 kwa mchango wake katika kuendeleza ajenda ya miundombinu barani Afrika na kusisitiza kuwa makubaliano yote yaliyofikiwa yanapaswa kutekelezwa kwa haraka ili yaweze kuleta manufaa ya moja kwa moja kwa wananchi.



 




Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu (MB) (Mwenye Suti) akisikiliza maelezo ya Huduma zinazopatikana katika banda la Mfuko wa PSSSF katika Maonesho ya Kilimo (Nanenane) Kanda ya Kusini yanayoendelea katika Viwanja vya Ngongo Manispaa ya Lindi Agosti 5, 2026

Mkurugenzi wa Utawala na Uendeshaji wa GST,  Neema  Mhagama akizungumza na waandishi wa habari  alipotembelea banda la GST katika Maonesho ya  Kilimo ya Kimatiafa Nane Nane yanayoendelea  kwenye Viwanja vya Dkt.John Samwel Malecela ,Nzuguni jijini Dodoma,
Na Mwandishi Wetu

TAASISI ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) imesema inaendelea kuwekeza katika mafunzo na ushirikiano na taasisi mbalimbali za kitaifa na kimataifa, ikiwa ni sehemu ya mikakati ya kuimarisha uwezo wa kitaalamu katika tafiti za jiosayansi na uchunguzi wa sampuli maabara.

Akizungumza wakati wa ziara katika Banda la GST kwenye Maonesho ya Kilimo ya Kimataifa Nane Nane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samwel Malecela, Nzuguni jijini Dodoma, Mkurugenzi wa Utawala na Uendeshaji wa GST, Neema Mhagama, amesema taasisi hiyo imekuwa ikiwajengea uwezo watumishi wake kupitia mafunzo na ushirikiano wa kitaalamu na taasisi za ndani na nje ya nchi

Amesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha GST inaendelea kuendana na mabadiliko ya teknolojia na kutumia mbinu za kisasa katika kufanya tafiti za jiosayansi pamoja na uchunguzi wa sampuli mbalimbali za miamba na madini.


“Ushirikiano huu umeendelea kuimarisha uwezo wa wataalamu wetu kwa kubadilishana uzoefu na teknolojia, jambo ambalo linaongeza tija katika shughuli za taasisi na kuchangia maendeleo ya Sekta ya Madini nchini,” amesema Mhagama.
Kwa mujibu wa Mhagama, GST imekuwa ikishirikiana na taasisi mbalimbali za ndani, zikiwemo Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), pamoja na taasisi za kimataifa kutoka Uingereza, Finland, Korea Kusini na pamoja na China.


Amesema kupitia mafunzo, programu za kubadilishana uzoefu na ushirikiano wa kitaalamu, wataalamu wa GST wameweza kupata maarifa na teknolojia mpya zinazochochea ubunifu na kuongeza ufanisi katika tafiti za jiosayansi

Ameongeza kuwa maarifa hayo yamekuwa na mchango katika kuboresha huduma zinazotolewa kwa wachimbaji, wawekezaji na wadau wengine wa Sekta ya Madini.

Aidha, Mhagama amewahimiza wadau wa Sekta ya Madini kutumia wataalamu wa GST katika shughuli zao za uchimbaji ili kupata taarifa sahihi kuhusu miamba, namna bora ya uchimbaji pamoja na uchukuaji na uchunguzi wa sampuli za miamba.

“Tunawahimiza wadau kutumia wataalamu wa GST ili kupata taarifa sahihi zitakazowawezesha kufanya uchimbaji wenye tija na kupunguza changamoto zinazoweza kujitokeza katika shughuli za uchimbaji,” amesema.

Vilevile, Mhagama amewaalika wananchi na wadau mbalimbali waliopo Dodoma na maeneo mengine nchini kutembelea Banda la GST katika Maonesho ya Nane Nane yanayoendelea jijini Dodoma, ili kupata elimu na kujifunza masuala mbalimbali yanayohusu jiolojia na madini.

Na Mwandishi Wetu
NIC Insurance imewahimiza wananchi kutumia fursa ya Bima ya Maisha ya Majaliwa katika kujiwekea malengo ya kifedha yatakayowasaidia baada ya kufikia muda walioujiwekea.

Hayo yamesemwa na Afisa Bima wa NIC Insurance, Thecla Mtege, wakati akizungumza na wananchi waliotembelea Banda la NIC Insurance katika Maonesho ya Kilimo ya Kimataifa yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samwel Malecela, Nzuguni jijini Dodoma.

Thecla amesema kupitia Bima hiyo, mwananchi anaweza kujiwekea malengo ya kifedha kwa muda anaouona unafaa, ikiwamo miaka mitano, 10 au zaidi, huku akichangia kiasi cha fedha anachokimudu kila mwezi.

Amesema utaratibu huo unamwezesha mwananchi kuweka akiba kwa ajili ya kutimiza malengo yake ya baadaye, kulingana na kiwango na muda alioujiwekea.

“Bima ya Maisha ya Majaliwa inamwezesha mwananchi kuchangia kiasi kidogo cha fedha kila mwezi kulingana na uwezo wake na malengo aliyojiwekea,” amesema Thecla.

Aidha, amesema iwapo mwananchi aliyekata Bima hiyo atafariki kabla ya kukamilisha muda wa Bima, NIC Insurance italipa kiasi cha Bima kwa wategemezi waliotajwa kwenye taarifa za Bima kwa kiwango kilekile kilichoainishwa.

Amesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha familia ya mwananchi aliyejiwekea mpango huo inaendelea kupata ulinzi wa kifedha hata endapo atafariki kabla ya kufikia muda wa kukamilisha malengo yake.

Dar es Salaam, Agosti 5, 2026 – Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira Tanzania (TRAMEPRO) limetoa wito kwa Serikali, wataalamu wa afya, wataalamu wa tiba asili, wakunga, wadau wa mazingira na jamii kwa ujumla kushirikiana katika kulinda afya na uhai wa mama na mtoto, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Wiki ya Unyonyeshaji Duniani yanayoendelea kuanzia Agosti 1 hadi 7, 2026.


Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, TRAMEPRO limesema linaungana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Shirika la Afya Duniani (WHO), UNICEF, Wizara ya Afya na wadau wengine wa afya duniani katika kuhamasisha unyonyeshaji wa maziwa ya mama kama njia muhimu ya kuboresha afya ya watoto na akina mama.

Shirika hilo limeeleza kuwa Wiki ya Unyonyeshaji Duniani ilianzishwa mwaka 1992 na World Alliance for Breastfeeding Action (WABA) kwa ushirikiano na WHO na UNICEF, kufuatia Azimio la Innocenti la mwaka 1990, lenye lengo la kulinda, kuhamasisha na kuunga mkono unyonyeshaji wa maziwa ya mama duniani.

Kwa mujibu wa TRAMEPRO, unyonyeshaji wa maziwa ya mama ni moja ya njia bora za kupunguza vifo vya watoto wachanga na kuboresha afya ya mama. Shirika hilo limeunga mkono mapendekezo ya WHO yanayosisitiza mtoto kuanza kunyonya ndani ya saa moja baada ya kuzaliwa, kupewa maziwa ya mama pekee kwa miezi sita ya kwanza, na kuendelea kunyonyeshwa pamoja na vyakula vya nyongeza hadi miaka miwili au zaidi.

TRAMEPRO pia limebainisha kuwa Tanzania hupata wastani wa watoto kati ya milioni 2.2 na 2.4 wanaozaliwa hai kila mwaka, huku Afrika ikichangia takribani asilimia 70 ya vifo vya akina mama duniani. Aidha, zaidi ya watoto wachanga milioni moja hufariki kila mwaka barani humo kutokana na sababu zinazoweza kuzuilika, ikiwemo kuzaliwa kabla ya wakati, maambukizi, kukosa hewa wakati wa kuzaliwa na utapiamlo.

Shirika hilo limeeleza kuwa afya ya mama na mtoto haiwezi kutenganishwa na mazingira bora, likisisitiza umuhimu wa upatikanaji wa maji safi, lishe bora, usafi wa mazingira, hewa safi na uhifadhi wa bioanuwai. Pia limefafanua kuwa mimea tiba, ambayo ni sehemu ya tiba asili, hutegemea mazingira salama na uhifadhi wa misitu pamoja na vyanzo vya maji.

Katika taarifa hiyo, TRAMEPRO limetoa wito maalumu kwa wataalamu wa tiba asili, wakunga wa jadi na wakunga wataalamu kuzingatia sheria, maadili ya taaluma na ushahidi wa kisayansi katika utoaji wa huduma. Pia limewahimiza kuwashauri wajawazito kuhudhuria kliniki mapema, kujifungulia katika vituo vya afya, kutambua dalili za hatari mapema na kushirikiana kwa karibu na wataalamu wa afya ili kuokoa maisha ya mama na mtoto.

Aidha, shirika hilo limetoa wito kwa Serikali kuendelea kuwekeza katika huduma za afya ya uzazi, kuongeza idadi ya wakunga na wahudumu wa afya, kuimarisha lishe, chanjo, maji safi na usafi wa mazingira, pamoja na kuwekeza katika tafiti za tiba asili salama.

TRAMEPRO pia limealika Wizara, taasisi za Serikali, mashirika ya kimataifa, asasi za kiraia, vyuo vikuu, taasisi za utafiti, sekta binafsi na washirika wa maendeleo kushirikiana katika kuendeleza tafiti, elimu ya afya, uhifadhi wa mimea tiba na ulinzi wa mazingira kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Shirika hilo limemalizia kwa kusisitiza kuwa kulinda afya ya mama na mtoto ni jukumu la kila mwananchi na kwamba ushirikiano kati ya sekta ya afya, tiba asili na uhifadhi wa mazingira ni msingi wa kujenga Taifa lenye watoto wenye afya, akina mama salama na maendeleo endelevu.

Top News