Na Mwandishi Wetu, Songea na Iringa

Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imewakutanisha wazabuni na Taasisi Nunuzi wa mikoa ya Ruvuma, Iringa na Njombe na kuwajengea uwezo kuhusu Moduli ya kupokea na kushughulikia Malalamiko na rufaa kwenye mfumo wa NeST kwa lengo la kuimarisha utendaji kazi. 

Mafunzo hayo yamefanyika kwa nyakati tofauti katika miji ya Songea na Iringa yamewahusisha washiriki 380 ambao ni wazabuni, wataalamu wa ununuzi, sheria, Tehama pamoja na makundi maalum yakiwemo wanawake, vijana, wazee na watu wenye mahitaji maalum pamoja na mafundi wa ndani.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando amesema mafunzo hayo yamekuwa yakitolewa na PPAA kwa kushirikiana na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) kwa lengo la kuwajengea uwezo wazabuni na Taasisi Nunuzi ili kuwapa ufanisi zaidi wakati wa utekelezaji wa majukumu yao, hususan katika kushughulikia malalamiko na migogoro itokanayo katika michakato ya ununuzi wa Umma. 

“Mafunzo haya yanalenga kuimarisha utendaji kazi wenu, kuhakikisha ufanisi, kuongeza uelewa wa matumizi ya Moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika wa Mfumo wa Ununuzi wa Umma kwa Njia ya Kielektroniki (NeST),” amesema Bw. Sando 

Bw. Sando ameongeza kuwa, katika kutimiza azma ya Serikali mafunzo yamewashirikisha vijana, wanawake na makundi maalum katika ununuzi wa umma ili kuwawezesha kupata elimu kuhusu ununuzi wa Umma hususan katika michakato ya ununuzi na kuhakikisha kuwa wanaisaidia Serikali kupata thamani halisi ya fedha katika miradi ya kimkakati yenye tija kwa Taifa.  

Pamoja na mambo mengine, Bw. Sando amewasihi washiriki kutumia mafunzo hayo kujifunza namna moduli ya kuwasilisha malalamiko na rufaa inavyofanya kazi katika Mfumo wa NeST kwani inatoa njia rahisi, ya haraka na yenye uwazi kwa wadau wote kushiriki katika mchakato wa ushughulikiaji wa malalamiko yanayotokana na michakato ya zabuni za umma. 

“Matumizi ya moduli yameongeza ufanisi katika usimamizi wa rufaa, kupunguza muda wa kushughulikia mashauri, na kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika utoaji wa haki, kuokoa muda na kupunguza gharama zinazohusiana na usuluhishi wa migogoro ya ununuzi,” ameongeza Bw. Sando

Kwa upande wake Meneja wa Usimamizi wa Rufaa na Sheria (PPAA), Bi. Florida Mapunda amesema kuwa mafunzo hayo yamelenga kutoa elimu kwa wadau wa ununuzi wa Umma kuhusu taratibu za uwasilishaji na ushughulikiaji wa malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST. 

“PPAA kwa kushirikiana na PPRA tumejenga moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko katika mfumo wa NeST ili kuwasaidia wadau wa ununuzi wa umma (Wazabuni na Taasisi za Umma) kuwasilisha malalamiko na rufaa kwa ufanisi zaidi kupitia mtandao,” amesema Bi. Mapunda.Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando akifungua mafunzo kuhusu Moduli ya kupokea na kushughulikia Malalamiko na rufaa kwenye mfumo wa NeST kwa wazabuni na Taasisi Nunuzi wa Mkoa wa Ruvuma. Kushoto ni Meneja wa Usimamizi wa Rufaa na Sheria (PPAA), Bi. Florida Mapunda na kulia ni Mkuu wa Sehemu ya Sheria PPAA, Bi. Agnes Sayi. Meneja wa Usimamizi wa Rufaa na Sheria (PPAA), Bi. Florida Mapunda akiwasilisha mada kuhusu uwasilishaji na ushughulikiaji wa malalamiko katika mfumo wa NeST kwa wazabuni na Taasisi Nunuzi walioshiriki mafunzo mkoani Ruvuma.
 Afisa Sheria kutoka PPAA, Bw. Venance Mkonongo akiwasilisha mada kuhusu uwasilishaji na ushughulikiaji wa malalamiko na rufaa katika ununuzi wa umma kwa wazabuni na Taasisi Nunuzi walioshiriki mafunzo mkoani Ruvuma.
Mkuu wa Sehemu ya Sheria PPAA, Bi. Agnes Sayi akiwasilisha mada kwa washiriki walioshiriki mafunzo kuhusu Moduli ya kupokea na kushughulikia Malalamiko na rufaa kwenye mfumo wa NeST kwa wazabuni na Taasisi Nunuzi wa Mikoa ya Iringa na Njombe. 
Mwezeshaji kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Bw. Daniel Kimaro akiwasilisha kuhusu utoaji wa tuzo, uandaaji, upekuzi, na utiaji saini wa mkataba kwa wazabuni na Taasisi Nunuzi wa Mikoa ya Iringa na Njombe. Sehemu ya wazabuni na Taasisi Nunuzi walioshiriki mafunzo kutoka Mikoa ya Iringa na Njombe

Viongozi wa PPAA wakiongozwa na Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando, katika picha ya pamoja na Kundi la wazabuni wenye mahiotaji maalum. Wengine pichani ni Meneja wa Usimamizi wa Rufaa na Sheria (PPAA), Bi. Florida Mapunda (kushoto)na kulia ni Mkuu wa Sehemu ya Sheria PPAA, Bi. Agnes Sayi.

 



Na Said Mwishehe,Michuzi TV-Njombe

MRADI wa kuzalisha umeme wa maji wa Lupali uliopo Kijiji cha Boimanda wilayani Njombe wenye uwezo wa kuzalisha kilowati 317 unaosimamiwa na Shirika la Benedictine Sisters of St. Gertrud Convent unatarajiwa kukamilika na kuingizwa katika gridi ya Taifa ndani ya miezi mitatu kuanzia sasa.

Katika kuufanikisha mradi huo Serikali kupitia Wakala wa Umeme Vijijini(REA) imetoa ruzuku ya fedha Sh.bilioni 5.4 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu mbalimbali ya mradi huo unaokwenda kuhudumia wananchi wa Wilaya hiyo.

Akizungumza leo Machi 11,2026 mbele ya Jukwaa la Wahariri Tanzania(TEF)wanaotembelea miradi ya REA ,Kaimu Meneja Usaidizi wa Kiufundi kwa Waendelezaji wa Miradi wa REA Mhandisi Emmanuel Yessaya amesema mradi huo ni sehemu ya uwekezaji wa sekta binafsi katika uzalishaji wa umeme utakaoingizwa katika gridi ya taifa kupitia Mkoa wa Njombe.

Amefafanua tayari miundombinu ya mradi huo imekamilika na kwasasa upo hatua za mwisho kuanza uzalishaji umeme ambao utaunganishwa katika gridi ya Taifa huku akifafanua mradi huo ulibuniwa na Shirika la Benedictine Sisters of St. Gertrud Convent kutokana na kukosekana umeme katika shirika hilo na vijijini jirani ingawa tayari REA imeshapeleka umeme.

“Miradi kama hii inasaidia kuongeza upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa wananchi na kuchochea shughuli za kiuchumi.Nitoe rai kwa wawekezaji kutumia fursa zilizopo kwenye maeneo yenye vyanzo vya maji kuanzisha miradi ya kuzalisha umeme.”

Amefafanua katika mikoa ya Njombe, Iringa na Ruvuma kuna vyanzo vya maji vingi ambavyo vinaweza kutumika kwa ajili ya miradi ya kuzalisha umeme,hivyo ni wakati muafaka kuchangamkia fursa na REA ipo tayari kushirikiana nao.

Kwa upande wake, Mratibu wa Mradi huo, Sister Imaculatha Mlowe kutoka Shirika la Benedictine Sisters of St. Gertrud Convent ameeleza ruzuku iliyotolewa na REA imesaidiakukamilisha ujenzi wa miundombinu ya mradi ikiwemo ujenzi wa intake weir, jengo la kuzalishia umeme,uwekaji wa mabomba ya kusafirisha maji, pamoja na kazi nyingine za ujenzi.

Pia amesema fedha iliyotolewa na REA imesaidia kugharamia tafiti za awali za mradi, ujenzi wa njia kuu za kusafirisha umeme za msongo wa kilovoti 11 zenye urefu wa kilomita 23.48 na njia ndogo za kusambaza umeme kwa watumiaji zenye urefu wa kilomita 30.61.

“Miundombinu ya kusafirisha na kusambaza umeme imeshakamilika na itaunganishwa gridi ya taifa kupitia TANESCO kwani tayari imefika katika kijiji jirani cha Kitulila.

“Hadi sasa wananchi zaidi ya 212 wa Kijiji cha Boimanda wameunganishwa na kupata huduma ya umeme kupitia gridi ya TANESCO wakati wananchi 366 wa Kijiji cha Matola wakipata umeme kupitia mradi wa zamani wa Lupali.”

Wakati huo huo Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Deodatus Balile, amesema mradi mradi huo unaonesha namna ushirikiano kati ya serikali na sekta binafsi unavyoweza kusaidia kuharakisha maendeleo ya kiuchumi nchini.

“Uzalishaji umeme ni moja ya vigezo muhimu vya maendeleo ya taifa kwani miradi ya aina hiyo itasaidia Tanzania kufikia malengo ya kuongeza uzalishaji wa umeme kutoka megawati 4,031 za sasa hadi kufikia megawati 8,000 ifikapo mwaka 2030.”











Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Machi 11, 2026 ameongoza Kikao cha kujadili Mapendekezo ya kufanya Maboresho ya Sheria ya Mapato ya baadhi ya Mifuko kilichofanyika kwenye ukumbi wa Waziri Mkuu, Bungeni jijini Dodoma, Machi 11, 2026.

Baadhi ya viongozi walioshiriki katika Kikao hicho ni pamoja na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, William Lukuvi, Waziri wa Ujenzi Abdallah Ulega, Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar, Waziri wa Madini, Anthony Mavunde na Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi.

Wengine ni Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Wanu Hafidh Ameir, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu- Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Ummy Nderiananga, Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Dkt. Jim Yonaz na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha Dkt. Natu El - maamry.









Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi, Ndg. Asha-Rose Migiro,leo tarehe 11 Machi 2026 amefanya mazungumzo jijini Dodoma na Balozi Parfait Onanga-Anyanga, Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Umoja wa Afrika na Mkuu wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa iliyopo Addis Ababa (UNOAU).

Balozi Onanga-Anyanga yupo nchini Tanzania kwa nafasi yake kama Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Mhe.António Guterres.

Kikao hicho ni sehemu ya mashauriano ya Mjumbe huyo na wadau mbalimbali wa kitaifa kwa lengo la kubadilishana mawazo kuhusu mustakabali wa kisiasa kufuatia Uchaguzi Mkuu wa tarehe 29 Oktoba, 2025, pamoja na juhudi pana za kuimarisha amani, demokrasia na mshikamano wa kitaifa nchini Tanzania.

Katika mazungumzo hayo, Ndg. Asha-Rose Migiro alisisitiza dhamira ya muda mrefu ya Tanzania katika kuendeleza utawala wa kidemokrasia, ushiriki wa kisiasa kwa njia ya amani na kuheshimu utawala wa sheria.

Alibainisha kuwa Tanzania inaendelea kuongozwa na misingi ya Mkataba wa Umoja wa Afrika wa Demokrasia, Uchaguzi na Utawala Bora, pamoja na viwango vya kimataifa vilivyowekwa katika Tamko la kimataifa la Haki za Binadamu na Mkataba wa kimatifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa.

Katibu Mkuu pia alieleza kuhusu mageuzi ya kisheria katika Tume ya Uchaguzi na taasisi nyingine yaliyofanyika kwa lengo la kuimarisha mfumo wa uchaguzi, ikiwa ni pamoja na kutungwa kwa sheria mpya za uchaguzi mwaka 2024 na hatua mbalimbali zilizolenga kuongeza uwazi, uwajibikaji na imani ya wananchi katika mchakato wa uchaguzi.

Mazungumzo hayo pia yaligusia matukio ya vurugu yaliyojitokeza katika baadhi ya maeneo nchini wakati na baada ya uchaguzi, ambayo yalisababisha upotevu wa maisha na uharibifu wa mali, ikiwemo mashambulizi dhidi ya ofisi za CCM. Ilibainishwa kuwa hatua stahiki zilichukuliwa kurejesha hali ya utulivu na amani nchini.

Pande zote mbili zilisisitiza umuhimu wa kuendelea kwa mazungumzo na maridhiano miongoni mwa wadau wa kitaifa. Hali kadhalika Katibu Mkuu wa CCM alimthibitishia Balozi Onanga-Anyanga kuwa Tanzania itaendeleza uhusiano wake na jumuiya ya kimataifa katika kuimarisha amani, usalama na maendeleo jumuishi.

CCM imepongeza ushirikiano madhubuti uliopo kati ya Tanzania na Umoja wa Mataifa na kuthibitisha dhamira yake ya kustawisha umoja wa kitaifa, utulivu na demokrasia katika Jamhuri ya Muungano ya Tanzania.






Na Mwandishi wetu - Dodoma 


Shirika la Maendeleo la Petroli Tanzania (TPDC) inaendelea kupanua miundombinu ya kusambaza gesi asilia kwa matumizi ya viwandani na majumbani katika Mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Lindi, Mtwara, na sasa mpango ni kufika Morogoro, Dodoma, Tanga, Kilimanjaro na Arusha.

Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi Mtendaji TPDC Mussa Makame akizungumza na Waandishi wa habari leo jijini Dodoma kutangaza Miradi ya Maendeleo na fursa za vijana kwa mwaka 2025/2026

 Makame amesema Vituo 14 vya kujaza gesi asilia (CNG) vimekamilika na vinahudumia vyombo vya usafiri ambapo lengo ni kuhamasisha matumizi ya gesi asilia, kupunguza utegemezi wa mafuta, na kuchangia katika kupunguza hewa ukaa. 

"TPDC inaunga mkono maono ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwa na asilimia 80 ya Watanzania wakitumia nishati safi ya kupikia ifikapo 2034"

Aidha Makame amesema hadi sasa, nyumba 2,515 zimeunganishwa na mtandao wa mabomba ya gesi asilia na tathmini ya kufikia maeneo mengine katika mikoa iliyofikiwa na bomba inaendelea ili kupanua wigo wa kuwafikia wateja.

Hata hivyo TPDC inashirikiana na Sekta binafsi kuanzisha miradi midogo ya gesi kimiminika (Mini-LNG) itakayowezesha kufikisha gesi asilia nchi nzima, na kuchangia katika maendeleo endelevu ya nchi.



 

Na Mwandishi wetu- Dodoma

Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali (GCLA) imefanikiwa kuwajengea uwezo vijana 8,086 katika uendeshaji wa shughuli zinazohusisha kemikali, na kuwasaidia kulinda afya zao na mazingira, Mafunzo hayo yamewezesha vijana kupata fursa za biashara katika usafirishaji wa kemikali na kuanzisha viwanda vidogo vidogo vya uzalishaji wa bidhaa za kemikali.

Dkt Fidelice Mafumiko Mkemia Mkuu wa Serikali ameyazungumza hayo leo jijini Dodoma katika Mkutano na Waandishi wa Habari kutangaza Miradi ya Maendeleo na fursa za vijana kwa mwaka 2025/2026

Mafumiko amesema Mamlaka imeendelea kuboresha miundombinu wezeshi, ikiwemo ujenzi wa majengo ya ofisi na maabara katika Ofisi ya Kanda ya Mashariki, jijini Dar es Salaam, wenye thamani ya Shilingi Bilioni 16.74, Ujenzi huo utaimarisha mazingira ya kufanyia kazi na utoaji huduma kwa wananchi.

 Pia amesema Mamlaka hiyo imekamilisha ujenzi wa nyumba za wafanyakazi katika mipaka ya Rusumo, Kabanga, Mutukula, Holili, na Namanga, wenye thamani ya Shilingi Bilioni 1.13, Juhudi hizo zinakusudia kuboresha mazingira ya kazi na makazi kwa wafanyakazi.

"Miradi hii imewasaidia vijana 260 kupata ajira, ikiwemo wataalam 27 na vibarua 233. Mamlaka inaendelea kuunga mkono sera za Serikali zinazohusiana na matumizi ya rasilimali za ndani (Local Content)"

Aidha Mafumiko amesema Mamlaka imeajili vijana 58 katika kazi za usafi wa mazingira na 38 katika ulinzi wa mali na majengo ya Mamlaka, hiyo inaonyesha jitihada za kuunda mazingira bora ya ajira kwa vijana.

Hata hivyo Katika kuimarisha matumizi ya TEHAMA, Mamlaka imeendelea kuboresha mifumo mbalimbali ya TEHAMA, na kukuza fursa kwa vijana katika sekta ya teknolojia.







Na Oscar Assenga,TANGA

KAMATI ya Siasa ya Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Tanga imeagiza kusimamishwa kazi Meneja wa Uwanja wa Mkwakwani Akida Machai kutokana na mapungufu mbalimbali yaliyobainika wakati wa ziara ya kamati hiyo kwa ajili ya kujionekana maendeleo yake.

Akizungumza kuhusu maamuzi hayo ,Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga Rajab Abdurhaman ambapo alisema kwamba ukiangalia mapato yanayopatikana na gharama ambazo zinatumika zikitolewa sawasawa na CCM hakuna chochote kinachopatikana lakini maji yanalipwa na CCM ,Umeme unalipwa na CCM.

Alisema wanafanya hivyo kuhakikisha wananchi waendelee kupata burudani ya michezo sasa wanapotoa fedha na kuona mambo bado hawaendi kama wanavyotarajia ni jambo ambalo limekuwa likiwaumiza.

“Mimi Binafsi nilitoa milioni 50 inawezekana fedha hamtafiti nyie ndio maana hamuoni uchungu wake mimi natayetafutaa fedha kwa wadau anawawaomba anajua uchungu wake lakini wao kwa sababu hawajui uchungu wake na walimuweka yeye kama meneja wakiamini angeweza kutusaidia kuhakikisha uwanja huo muda wote unaweza kuwa bora unatumika”Alisema

“Lakini ukija wakati wote uwanja umekuwa kama Mbuga za Wanyama haiwezekani sio sawa mpaka leo viti vimeletwa havijafungwa na mmeviacha mpaka vimeota majani”Alisema
Aidha alisema kwamba wao wamekaa kama viongozi waliochaguliwa ili uwanja uweze kufikia vigezo lakini mpaka kufikia wakati uwanja kufungiwa na TFF hivyo hawawezi kukubali.

“Nilisema kwa hali ilivyo muda wowote TFF wangeweza kuja kutufungia uwanja hivyo nitoe maelekezo kwa Kamati ya Siasa mkoa kaeni Mtafute Meneja mwengine ili changamoto hizo ziweze kuondoka”Alisema

Hata hivyo alisema kwamba kwa mpangaji Yule mwenye baa pale nje ambayo haijakidhi vigezo na Shirikisho la Soka nchini (TFF) walishasema ile baa inazuia washabiki kuingia uwanjani wakati wa mpira na inatakiwa kuondoka lakini mpaka leo haijaondoka.
“Maanake huyo mtu ana mapembe kiasi gani yeye ni mpangaji kwenye eneo letu lakini anakigomea CCM hivyo nahitaji hii baa leo iondoke ili maelekezo na maagizo ya TFF tuweze kuyatimiza na apatikane Meneja mwengine haraka ili aweze kushirikina na vongozi wa CCM kufungwa viti hivyo na nanatoa mwezi mmoja”Alisema

Awali akizungumza aliyekuwa Meneja wa uwanja wa CCM Mkoa wa Tanga Akida Machai alisema changamoto ya uhaba wa nguvu kazi ndio imepelekea kukwamisha viti hivyo kufungwa .

Alisema kwamba walikuwa wakihitaji kuongezewa nguvu kazi yeye anashukru CCM kwa nafasi waliompatia na wanamtakia kilala heri Meneja Mpya huku akieleza wakati viti vilipokuja walipeleka Bajeti ya kufunga viti CCM na vitu vinavyohusika na hawezi kutoa fedha zake kufungwa viti.

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, tarehe 11 Machi 2026 amepokea salamu maalum kutoka kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres, zilizowasilishwa kwake na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu huyo, Bw. Parfait Onanga-Anyanga, katika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma.

Mjumbe huyo maalum yuko nchini Tanzania kwa ziara ya kusikiliza maoni ya wadau mbalimbali na kutathmini hatua zinazochukuliwa na Serikali katika kuimarisha utulivu wa kisiasa, mshikamano wa kitaifa na kuendeleza misingi ya utawala wa sheria kufuatia matukio ya uvunjifu wa amani yaliyotokea kabla na wakati wa Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025.

Akizungumza baada ya kukutana na Rais Samia, Bw. Onanga-Anyanga amesema Umoja wa Mataifa unatambua na kupongeza hatua zinazochukuliwa na Serikali ya Tanzania kufuatia matukio hayo, hususan uamuzi wa kuunda Tume Huru ya Uchunguzi pamoja na dhamira ya kufanya mazungumzo jumuishi ya kitaifa na kuendeleza mchakato wa mabadiliko ya Katiba.

Ameeleza kuwa Tanzania inaendelea kutambuliwa na Umoja wa Mataifa kama nchi yenye historia ya muda mrefu ya amani, utulivu wa kisiasa na mshikamano wa kitaifa, huku pia ikithaminiwa kwa mchango wake katika juhudi za kulinda na kuimarisha amani barani Afrika.

Katika ziara yake nchini, Bw. Onanga-Anyanga amekutana na viongozi wa taasisi mbalimbali ikiwemo Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mahakama ya Tanzania, Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa pamoja na viongozi wa vyama vya siasa.

Aidha, amefanya mazungumzo na Mwenyekiti na wajumbe wa Tume Huru ya Uchunguzi pamoja na wadau wengine wa kisiasa na kijamii ili kupata maoni na mitazamo tofauti kuhusu matukio yaliyotokea na hatua zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali.

Bw. Onanga-Anyanga amesema mashauriano hayo yatauwezesha Umoja wa Mataifa kupata taswira halisi ya matukio ya Oktoba 29, 2025 pamoja na juhudi zinazofanywa na Serikali ya Tanzania katika kutatua changamoto zilizojitokeza wakati na baada ya uchaguzi huo.

Ameongeza kuwa hatua hizo zina mchango muhimu katika kuimarisha maridhiano ya kitaifa, kurejesha imani ya wananchi na kuendelea kujenga taasisi imara za kidemokrasia nchini. Aidha ameahidi kuwasilisha tathmini ya mashauriano hayo kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ili kuendelea kuimarisha mashauriano kati ya Umoja wa Mataifa na Tanzania.

Kwa upande wake, Rais Samia Suluhu Hassan ametoa salamu za shukrani kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kwa kutuma ujumbe maalum nchini Tanzania ili kupata uelewa wa kina kuhusu hali ya nchi na kusikiliza maoni ya wadau mbalimbali.

Rais Samia amesema Serikali ya Tanzania imejizatiti kuhakikisha mchakato wa kufuatilia matukio hayo unafanyika kwa kuzingatia misingi ya utawala wa sheria, uwajibikaji na haki, huku ikiendelea kulinda amani, umoja wa kitaifa na utulivu wa kisiasa ambao umekuwa msingi muhimu wa maendeleo ya nchi.

Aidha, amesema Serikali iko tayari kupokea na kuyafanyia kazi mapendekezo yatakayowasilishwa na Tume Huru ya Uchunguzi mara baada ya kukamilika kwa kazi yake, akieleza kuwa mapendekezo hayo yatakuwa sehemu muhimu ya kuimarisha maridhiano ya kitaifa na mchakato wa marekebisho ya Katiba.

Rais Samia pia amesisitiza kuwa Tanzania itaendelea kushirikiana na Umoja wa Mataifa pamoja na jumuiya nyingine za kimataifa katika kukuza demokrasia, utawala bora na maendeleo jumuishi kwa manufaa ya wananchi.


📍Kibaha, Pwani – Machi 11, 2026
WAJUMBE wa Baraza la Wafanyakazi wa Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA) wametakiwa kuzingatia uadilifu, uwazi na weledi katika kuwasilisha na kushughulikia changamoto za watumishi wanaowawakilisha, ili kuongeza ufanisi na tija katika utendaji kazi wa taasisi.

Wito huo umetolewa leo Machi 11, 2026 na Meneja wa Fedha na Mipango wa PBPA, Bw. Kedron Mbwilo, alipokuwa akizungumza kwa niaba ya Mtendaji Mkuu wa PBPA wakati wa ufunguzi wa Kikao cha Pili cha Baraza la Wafanyakazi kilichofanyika katika ukumbi wa Chuo cha Uongozi cha Mwalimu Nyerere, Kibaha mkoani Pwani.

Amesema Baraza la Wafanyakazi ni jukwaa muhimu linalounganisha menejimenti na watumishi, hivyo wajumbe wanapaswa kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu na uwajibikaji mkubwa ili kuhakikisha masuala ya watumishi yanawasilishwa na kutatuliwa ipasavyo.

“Baraza la Wafanyakazi ni kiunganishi muhimu kati ya menejimenti na watumishi. Ni wajibu wa wajumbe kuwa waadilifu na kuwawakilisha watumishi wenzao kwa weledi mkubwa ili kuongeza tija na ufanisi katika taasisi,” amesisitiza Bw. Mbwilo.

Aidha, amewahimiza watumishi wa PBPA kuendelea kufanya kazi kwa ushirikiano na kujituma ili kuunga mkono jitihada za Serikali katika kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050, ambayo kwa upande wa sekta ya nishati inalenga kuhakikisha Tanzania inakuwa na upatikanaji wa uhakika wa nishati ya mafuta, miundombinu imara ya mafuta pamoja na usimamizi bora wa rasilimali za petroli.

Kwa upande wake, Kaimu Meneja wa Rasilimali Watu wa PBPA, Bw. Matiko Sanawa, amewahimiza wajumbe wa baraza hilo kutumia kikao hicho kama fursa ya kujadili kwa uwazi maoni, mapendekezo na changamoto mbalimbali zitakazochangia kuimarisha uendeshaji wa taasisi.

Amefafanua kuwa kikao hicho cha Baraza la Wafanyakazi kinafanyika kwa mujibu wa matakwa ya kisheria na kwamba, pamoja na mambo mengine, kitajadili taarifa ya utekelezaji wa Mpango Kazi na Bajeti kwa kipindi cha Julai 2025 hadi Desemba 2026, pamoja na kuwasilishwa kwa rasimu ya Mpango Kazi wa PBPA kwa kipindi cha 2026/2027 hadi 2030/2031 na rasimu ya Bajeti ya PBPA kwa mwaka wa fedha 2026/2027.




Top News