Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) anayeshughulikia Sera za Uchumi na Fedha, Dkt. Yamungu Kayandabila, amesema kuwa mifumo ya malipo ya Taifa ina mchango mkubwa katika kukuza uchumi jumuishi na kuimarisha ujumuishwaji wa kifedha nchini.
Akitoa hotuba ya ukaribisho kwa wanafunzi wa Shahada ya Uzamili ya Biashara (MBA) kutoka Chuo Kikuu cha Stanford, Marekani, waliotembelea BoT jijini Dar es Salaam, Dkt. Kayandabila alieleza kuwa mifumo ya malipo inachangia ukuaji wa uchumi shirikishi kwa kuwezesha malipo ambayo yanachochea ugavi katika uchumi na kuwa uti wa mgongo wa Uthabiti wa Sekta ya Fedha.
Alibainisha kuwa mifumo ya malipo yenye ufanisi, iliyo salama na shirikishi huchochea ufanisi wa sera ya fedha kwa kuwezesha uenezaji mzuri wa mabadiliko ya viwango vya riba vya Benki Kuu na kuimarisha udhibiti wa ukwasi ndani ya uchumi.
Dkt. Kayandabila alisema Benki Kuu imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kisera na kuwekeza katika miundombinu ili kuimarisha na kuboresha mifumo ya malipo, sambamba na kuchochea ubunifu hususan katika huduma za kifedha za kidijitali na ujumuishwaji wa kifedha.
Akifafanua kuhusu historia ya maboresho hayo, alisema kuwa mchakato wa kisasa wa mifumo ya malipo ulianza katikati ya miaka ya 1990 kama sehemu ya mageuzi mapana ya sekta ya fedha yaliyolenga kuongeza ufanisi, usalama na uthabiti wa mfumo wa fedha.
Aliongeza kuwa mageuzi hayo yaliwezesha kuingia kwa benki binafsi za ndani na za kimataifa, ubinafsishaji wa baadhi ya benki za serikali pamoja na kuondolewa kwa baadhi ya vikwazo katika huduma na bidhaa za kifedha.
Kwa mujibu wa Dkt. Kayandabila, mwaka 1996 BoT ilianzisha Mradi wa Maboresho ya Mifumo ya Malipo ya Taifa uliolenga kubadilisha mfumo wa zamani uliotegemea zaidi fedha taslimu na karatasi kuwa mfumo wa kielektroniki unaoendana na viwango vya kimataifa.
Alikumbusha kuwa kabla ya maboresho hayo, matumizi ya fedha taslimu yalitawala, huku hundi zikichukua hadi siku 14 kukamilisha miamala mikoani na siku 7 jijini Dar es Salaam, hali iliyokuwa ikichelewesha shughuli za kiuchumi.
Aidha, alisisitiza kuwa BoT inaendelea kufuatilia maendeleo ya teknolojia za mifumo ya malipo duniani na kushirikiana na wadau wa kikanda na kimataifa ili kunufaika na ubunifu huo, huku ikiendelea kulinda uthabiti wa sekta ya fedha, uadilifu wa mifumo na maslahi ya watumiaji.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Mifumo ya Malipo ya Taifa, Bi. Lucy Shaidi, akielezea hatua muhimu zilizofikiwa katika safari ya kuendeleza mifumo ya malipo hadi kufikia mwaka 2025, alisema kuwa kumekuwapo na ukuaji wa kasi wa malipo ya papo kwa papo, huduma za fedha kupitia simu za mkononi, pamoja na mifumo ya malipo inayoweza kuunganishwa.
Alibainisha kuwa maendeleo hayo yanaendelea kuichochea Tanzania kuelekea katika mfumo wa fedha uliojumuishi zaidi, wenye ufanisi, na unaotegemea kwa kiasi kikubwa teknolojia za kidijitali.
Miongoni na mafanikio makubwa ya Benki Kuu katika mifumo ya malipo ni kuanzishwa kwa Mfumo wa Malipo ya Papo kwa Hapo (Tanzania Instant Payment System – TIPS) unaoruhusu watumiaji wa huduma za fedha kutuma na kupokea fedha papo hapo , bila kujali taasisi ya kifedha wanayotumia.
TIPS umeongeza ufanisi, umepunguza gharama za miamala, na kuimarisha ujumuishwaji wa kifedha kwa kurahisisha miamala ya kifedha kwa watu binafsi na biashara nchini Tanzania.
WALIMU 150 wa amali kwenye shule za serikali wanaondoka Jumapili kwenda nchini India kwa mafunzo maalum ya amali ambayo yatawawezesha kuongeza ujuzi kwenye taaluma hiyo.
Walimu hao kutoka mikoa mbalimbali nchini waliagwa rasmi jana kwenye hafla maalum iliyohudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali.
Waliagwa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolph Mkenda na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, TAMISEMI, Profesa Riziki Shemdoe na Mkurugenzi Mkuu wa Global Education Link, (GEL) Abdulmalik Mollel.
Akizungumzawakati wa hafla ya kuwaaga walimu hao, Profesa Mkenda alisema safari hiyo ni maono ya Rais Samia Suluhu Hassan ambaye amekuwa akisisitiza kuboreshwa kwa elimu ya amali.
Profesa Mkenda alisema kwa kuwa wameanza kutoa mafunzo hayo ya amali ikiwemo kwenda kujifunza kwenye mataifa mbalimbali duniani hakutakuwa na kurudi nyuma.
“Mheshimiwa Rais Samia amesisitiza mara kadhaa kuhusu mafunzo ya amali, anataka kuona tunakwenda mbali zaidi namimi nasema kwa kuwa tumeanza basi hatutarudi nyuma, tutakwenda India na mataifa mbalimbali kujifunza wenzetu wamefanyanini kwenye mafunzo ya amali,” alisema
Aidha, aliwataka walimu hao kujifunza kwa bidii wakiwa nchini India ili watakaporudi wawe mfano kwa walimu wengine ambao hawajapata nafasi hiyo.
“Tunataka kuona mabadiliko makubwa, mtakaporudi watu waone kabisa kwamba kuna watu walikuwa nchini India kwa masomo, mhakikishe shule zinavifaa vya kufundishia masomo ya amali katika ngazi zote,” alisema
“Tunatambua maono makubwa ya rais wetu kwenye masomo ya amali kwa hiyo kazi yetu sisi wasaidizi wake ni kuyatafsiri kwa vitendo kwa kufanya kazi kuhakikisha tunatimiza ndoto hizo kwa kutoa elimu bora na siyo bora elimu,” alisema
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, TAMISEMI, Profesa Riziki Shemdoe alisema kuzingatia nidhamu na maadili watakayofundishwa nchini India kwaajili ya kuja kuleta matokeo chanya kwenye maeneo yao.
“Tunataka mkirudi muwe chachu kwa wengine kutaka nao kwenda India kujifunza, mtushauri tufanye nini ili tuweze kutoa matokeo chanya kwenye maono ya rais Samia,” alisema
Aidha, alisema safari ya walimu hao ni matokeo ya mabadiliko ya mitaala ya elimu yaliyoanza muda mrefu na kuja kutekelezwa na Rais wa awamu ya sita, Rais Samia Suluhu Hassan.
“Mageuzi ya elimu utekelezaji wake ni wa muda mrefu,unamilima na mabonde kwa hiyo ingawa kuna changamoto nyingi lakini sisitutapambana mpaka mwisho hakutakuwa na kurudi nyuma hata siku moja,” alisema Waziri Shemdoe









Dar es Salaam
KAMPUNI ya Airtel Tanzania imezindua rasmi mnara wa mawasiliano wenye teknolojia ya 4G na 5G katika mtaa wa Machimbo, Tabata, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kampuni hiyo kuboresha huduma za mawasiliano na kukuza uchumi wa kidijitali kwa wananchi.
Akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi, Afisa Mtendaji wa Kata ya Machimbo, Bi. Lidya Bwathondi, alisema kuwa uwekezaji huo umeleta mabadiliko makubwa kwa wakazi wa eneo hilo ambao awali walikumbana na changamoto za mawasiliano.
“Kabla ya ujio wa mnara huu, wakazi wa Machimbo walikuwa wanapata shida kupata mawasiliano ya uhakika. Leo hii hali imebadilika, mawasiliano yameimarika na wananchi wanaweza pia kufanya biashara zao mtandaoni kwa urahisi zaidi,” alisema Bwathondi.
Kwa upande wake, Meneja Biashara wa Airtel, Bw. Benson Mbwanga, alieleza kuwa uzinduzi wa mnara huo ni sehemu ya mkakati wa Airtel wa kuendelea kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi pamoja na kuunga mkono jitihada za Serikali katika kuimarisha miundombinu ya mawasiliano nchini.
“Uwekezaji huu unaonesha dhamira ya Airtel ya kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma bora za mawasiliano. Tunaendelea kupanua mtandao wetu wa 4G ili kuwezesha wananchi kuwasiliana kwa urahisi, kufanya biashara za kidijitali na kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kisasa,” alisema Mbwanga.
Baadhi ya wakazi wa mtaa wa Machimbo, akiwemo Bi. Mariam Simon, Bi. Bertha Livingston, Bi. Khadija Seif na Bi. Sada Nyambe, walieleza kufurahishwa kwao na uwekezaji huo wakisema utarahisisha shughuli zao za kila siku, hususan biashara za kidijitali, na kuishukuru Airtel kwa kuchagua kuwekeza katika eneo lao.
Uzinduzi wa mnara huu ni sehemu ya uwekezaji mpana wa Airtel ambapo jumla ya minara mipya tisa yenye teknolojia ya 4G imejengwa jijini Dar es Salaam, ikiwa ni jitihada za kuendelea kuboresha huduma za mawasiliano na kusaidia maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.
Airtel Tanzania inaendelea kujikita katika kutoa huduma bora, za uhakika na zenye ubunifu, huku ikiunga mkono juhudi za Serikali za kuhakikisha upatikanaji wa mawasiliano bora kwa Watanzania wote.

Mbunge wa Jimbo la Kilombero, Abubakari Asenga, ametoa pole kwa wananchi wa jimbo hilo waliokumbwa na mafuriko makubwa yaliyosababishwa na mvua zinazoendelea kunyesha katika maeneo mbalimbali ya Halmashauri ya Mji wa Ifakara, mkoani Morogoro.
Akizungumza leo Machi 27, 2026 katika Ofisi ya Waziri Mkuu inayoshughulikia maafa, Mara baada ya kupokea msaada wa magodoro, mablanketi na chakula, Asenga amesema kuwa juhudi zinaendelea kuhakikisha wananchi waliopata madhara wanapata msaada wa haraka ili kupunguza athari walizokumbana nazo.
Mbunge huyo ameeleza shukrani zake kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, pamoja na Waziri Mkuu, Mwigulu Nchemba, kwa kuwezesha upatikanaji wa vifaa vya dharura kwa ajili ya kuwasaidia waathirika.
Amesema kuwa tayari wamepokea msaada unaojumuisha magodoro 75, mablanketi pamoja na tani 10 za mahindi, ambavyo vitasambazwa kwa wananchi waliokumbwa na mafuriko hayo wakati wakisubiri hatua zaidi za msaada kutoka serikalini.
Aidha, Asenga amewapongeza wananchi pamoja na kamati ya maafa ya wilaya kwa kushirikiana na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kwa juhudi kubwa walizozifanya kuokoa maisha ya watu. Amebainisha kuwa hadi sasa hakuna taarifa yoyote ya vifo iliyothibitishwa licha ya uharibifu mkubwa wa makazi ya wananchi.
Ameongeza kuwa baada ya kupokea taarifa za kuwepo kwa wananchi wasio na mahali pa kulala, ofisi yake ilichukua hatua za haraka kutafuta msaada wa magodoro, mablanketi pamoja na chakula ili kuhakikisha mahitaji muhimu yanapatikana kwa wakati.
Kwa upande mwingine, amesema ofisi ya mbunge imefanikiwa pia kupata unga ambao unatarajiwa kusambazwa kesho Jumamosi katika maeneo yaliyoathirika zaidi ikiwemo Ifakara, Lumemo na Michenga, ili kuwafariji na kuwasaidia wananchi waliokumbwa na adha hiyo.
Asenga amesisitiza kuwa wataendelea kuisimamia serikali kuhakikisha inatekeleza mipango ya kudhibiti athari za mafuriko, ikiwemo kufufua mabwawa, kupanua mito pamoja na kujenga miundombinu ya kinga kama matuta ili kupunguza madhara ya mafuriko siku zijazo.
Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa, takribani kaya 100 zenye jumla ya watu wapatao 500 zimeathirika na mafuriko hayo. Ingawa baadhi ya maeneo yameanza kupungua maji na wananchi kurejea makwao, bado wapo ambao hawajaweza kurudi kutokana na kiwango kikubwa cha maji kilichoingia kwenye makazi yao.
Kwa ujumla, juhudi za serikali zinaendelea kusaidia waathirika wa mafuriko katika Jimbo la Kilombero, huku msisitizo ukiwa ni kuhakikisha misaada ya dharura inawafikia wananchi wote walioathirika na kuweka mikakati madhubuti ya kudhibiti majanga kama haya siku zijazo.
SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) kwa kushirikiana na Tume ya Ushindani (FCC) wamekutana na wadau wa bidhaa za pombe nchini kwa lengo la kuwajengea uelewa juu ya matakwa ya sheria, kanuni na viwango vinavyosimamia sekta hiyo.
Kikao hicho kilichofanyika leo Machi 27, 2026 jijini Dar es Salaam, pia kimelenga kujadiliana na kubaini changamoto zinazowakabili wadau katika kukidhi matakwa ya kisheria pamoja na masuala ya ushindani, ili kupata ufumbuzi wake.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao hicho, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TBS, Mhandisi Yona Afrika, amesema kumekuwa na malalamiko yanayopokelewa na taasisi hizo kuhusu uwepo wa pombe duni na bandia katika soko, hali inayochangiwa na baadhi ya wafanyabiashara wasio waaminifu.
“Bidhaa hizi zisipozingatia matakwa yaliyowekwa, zinaweza kuhatarisha afya na usalama wa walaji,” amesema Afrika.
Ameongeza kuwa TBS kwa kushirikiana na FCC zitaendelea kuimarisha usimamizi wa viwango ili kudhibiti ubora wa bidhaa pamoja na kuhakikisha ushindani wa haki katika soko.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi.Roberta Feruzi, amesema uwepo wa pombe duni na bandia si tu unaharibu ushindani wa haki bali pia husababisha malalamiko kutoka kwa walaji kuhusu thamani ya fedha wanazolipa na athari za kiafya.
Amebainisha kuwa hali hiyo pia hudhoofisha biashara halali na kuvuruga mazingira ya ushindani sawa kwa wafanyabiashara wanaofuata sheria.









































