Na Ashura Mohamed, ARUSHA.

Naibu Mkuu wa Chuo, Upande wa Taaluma, Utafiti na Ushauri wa Kitaaluma kutoka Chuo cha Uhasibu Arusha IAA, Dkt. Grace Temba, ameweka jiwe la msingi kwa ajili ya maandalizi ya kongamano la kimataifa la utalii linalotarajiwa kufanyika tarehe 25 Septemba, 2026 mkoani Arusha.

Tukio hilo la kongamano ni muhimu kwa taasisi hiyo na maalum kwa wadau wa utalii kutoka maeneo mbali mbali duniani likilenga wadau wa sekta ya utalii kwa dhima kubwa ya kuhamasisha utalii wa ndani ili kuendelea kuhamasisha idadi ya watalii kuongezeka.

Akizungumza mara baada ya uzinduzi huo Dkt. Grace amesema kuwa lengo hasa ni kuhakikisha wadau mbali mbali wanashiriki na kufanya kongamano hilo kujumlisha watunga sera, wadau wa utalii kutoka ndani na nje ya nchi kujiandaa na kushiriki kwa ufanisi zaidi.

“Siku ya kongamano tunawaweka pamoja wadau mbali mbali tunatoa taarifa mbali mbali za utafiti zilizofanywa na wadau mbali mbali waliopo katika sekta ya utalii lakini pia Chuo cha Uhasibu Arusha, watunga sera wa taasisi na mlaji ili kuja na suluhisho na maboresho makubwa katika sekta ya utalii kwa lengo la kunufaisha pande zote,” alisema Dkt. Grace.

Aidha amesema kuwa kongamano hilo la nne linatarajiwa kuendelea kukuza na kutangaza nchi kimataifa kwa kuja na mawasilisho ambayo yatalenga wadau na watoa huduma kuendelea kujikuza kimasoko, miundombinu, na kuifanya sekta hiyo kuwa bobezi na kuchangia pato la taifa.

Nae Kaimu Mkuu wa Kitivo cha Biashara na Sayansi ya Jamii kutoka Chuo cha Uhasibu Arusha IAA, Bi. Lorna Boniface Mwijarubi, amesema kuwa chuo hicho kinatarajia kushirikiana na taasisi mbali mbali na wadau wa utalii katika kuonyesha tafiti na bunifu ambazo zitaisaidia sekta ya utalii kuwa bora zaidi na kuendelea kuliingizia taifa kipato.

Amesema kuwa mafanikio yaliyopatikana kutokana na makongamano yaliyopita ni makubwa kwa kuwa yamekijengea chuo mashirikiano na wadau ambayo huwezesha wanafunzi wa kozi ya utalii na ukarimu kupata fursa ya kujifunza kwa vitendo katika maeneo mbali mbali nchini na kusaidia kupata ajira pamoja na taifa kupata mapato kupitia sekta hiyo.

Chuo cha Uhasibu Arusha IAA kimeendelea kuwa maarufu katika sekta mbali mbali kwa kutoa elimu bora yenye ushindani sokoni huku katika sekta ya utalii inatajwa kuwa ndio chuo pekee kinachotoa kozi ya utalii na ukarimu nchini ambayo inatajwa kuwa na mchango mkubwa katika kutangaza nchi na kuendelea kuifanya sekta hiyo kuwa bora zaidi nchini.

Kaimu Mkuu  wa  chuo Upande wa Taaluma,Utafiti na   Ushauri wa kitaaluma kutoka cha Uhasibu Arusha(IAA), Dkt.Grace Temba Akiwa katika hafla hiyo iliyofanyika chuoni hapo.
Meneja Masoko na Ushirikiano na Mashirika kutoka hoteli ya Mount Meru Arusha bi.Lucy Foya akiwa katika hafla hiyo iliyofanyika chuo Cha Uhasibu Arusha
Wadau Mbali Mbali wakiwa katika picha ya Pamoja chuoni hapo


Na: Farida Mangube

Ufugaji wa ng’ombe wa maziwa katika Kata ya Igima, Wilaya ya Wanging’ombe mkoani Njombe, umeendelea kuwa chanzo kikuu cha mabadiliko ya kiuchumi kwa wananchi, baada ya uzalishaji kuongezeka na ubora wa maziwa kuboreka kutokana na elimu na utafiti unaotolewa na wataalamu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA).

Afisa Mifugo wa Kata ya Igima, SHAZI MOSES OKALA, amesema kata hiyo ina zaidi ya wafugaji 300 wa ng’ombe wa maziwa wenye zaidi ya ng’ombe 700, ambapo kwa sasa huzalisha zaidi ya lita 2,500 za maziwa kwa siku. Amesema maziwa hayo hukusanywa kupitia vituo vya ukusanyaji kabla ya kupelekwa kwenye kituo cha kupoozea na baadaye kusafirishwa kwa ajili ya usindikaji.

Yokara amesema kabla ya kuanza kwa elimu na utafiti wa wataalamu wa SUA kupitia Mradi wa NANOCOM, wafugaji walikuwa wakikabiliwa na changamoto ya magonjwa ya mifugo hususan homa ya kiwele (mastitis), hali iliyosababisha maziwa mengi kuchachuka na kupoteza ubora wake. Hata hivyo, ameeleza kuwa hali hiyo imepungua kwa kiasi kikubwa baada ya wafugaji kupewa elimu ya usafi wa mabanda na mbinu bora za ufugaji.

Ameongeza kuwa elimu hiyo imechangia si tu kuboresha afya ya mifugo, bali pia kuongeza uzalishaji wa maziwa na kipato cha wafugaji, ambapo sasa maziwa mengi yanakidhi viwango vya soko tofauti na ilivyokuwa awali.

Katika hatua nyingine, mfugaji na kiongozi wa kikundi cha Beach Group, Bi. Liones Richard, ameeleza jinsi ufugaji ulivyobadilisha maisha yake tangu alipoanza mwaka 2007 akiwa na ng’ombe mmoja pekee, ambapo kwa sasa anamiliki ng’ombe wanne wanaozalisha zaidi ya lita 20 za maziwa kwa kila ng’ombe kwa siku.

Bi. Liones amesema mafanikio hayo yametokana na matumizi ya mbinu bora za ufugaji na ushauri wa kitaalamu anaoupata, ambao umemsaidia kuboresha lishe ya mifugo, afya ya ng’ombe na usafi wa mabanda, hivyo kuongeza uzalishaji kwa kiwango kikubwa.

Amehitimisha kwa kusema kuwa mafanikio hayo yamemuwezesha kujenga nyumba bora na kuwapatia watoto wake elimu, huku akiwahamasisha wanawake, vijana na wafugaji wengine kuona ufugaji wa ng'ombe wa maziwa kama fursa muhimu ya kiuchumi inayoweza kubadilisha maisha endapo itafanyika kwa weledi na maarifa sahihi.





Historia ya Tanzania katika harakati za kupigania uhuru, kuundwa kwa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar pamoja na mchango wake katika ukombozi wa Afrika ni miongoni mwa vivutio vitakavyopewa nafasi ya kipekee katika Maonesho ya Kiswahili yatakayofanyika jijini Paris, Ufaransa, sambamba na Kongamano la Pili la Kiswahili la Kimataifa.

Maonesho hayo yatakayofanyika katika viunga vya Makao Makuu ya UNESCO kuanzia Julai 4 hadi 7, 2026, yanatarajiwa kuwakutanisha washiriki kutoka mataifa mbalimbali duniani kwa lengo la kuendeleza matumizi ya Kiswahili na kuonesha mchango wake katika amani, mshikamano na diplomasia ya uchumi duniani.

Kwa mujibu wa mwongozo wa kongamano hilo, sehemu maalum ya maonesho itajikita katika kuonesha historia ya uhuru wa Tanzania, hatua za kuundwa kwa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar pamoja na nafasi ya Tanzania katika kuunga mkono harakati za ukombozi wa mataifa mbalimbali ya Afrika yaliyokuwa chini ya ukoloni.

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) ni miongoni mwa taasisi za Serikali chini ya Wizara ya Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo, zitakazotuma uwakilishi wa kushiriki kwa mara ya kwanza katika kongamano hilo.

Akizungumza jijini Dar es Salaam tarehe 11 Juni, 2026 kuhusu Kongamano hilo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Wakili Patrick Kipangula, amesema lengo la kutuma uwakilishi wa Taasisi ni kujifunza uzoefu wa kimataifa, kuimarisha ushirikiano na wadau wa lugha na vyombo vya habari kutoka mataifa mbalimbali pamoja na kuendeleza mchango wa Tanzania katika kukuza Kiswahili.

Washiriki watapata fursa ya kujifunza mchango wa Tanzania katika kujenga mshikamano wa Afrika na kuimarisha ushirikiano wa kimataifa kupitia diplomasia, huku vielelezo mbalimbali vikionesha nafasi ya taifa hilo kama kitovu cha harakati za ukombozi wa Bara la Afrika.

Katika kuongeza mvuto wa maonesho hayo, nukuu za viongozi mashuhuri wa Tanzania, akiwemo Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, zitaoneshwa kupitia skrini kubwa kwa lengo la kuhamasisha maadili ya uongozi, amani, umoja na maendeleo.

Aidha, maonesho hayo yataangazia mchango wa lugha ya Kiswahili katika diplomasia ya Afrika na nafasi yake katika kuimarisha utangamano wa watu wa mataifa mbalimbali, sambamba na juhudi zinazoendelea za kukitangaza Kiswahili kama lugha ya kimataifa inayobeba historia, utamaduni na utambulisho wa Waafrika.

Kongamano la Pili la Kiswahili la Kimataifa linaandaliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na UNESCO chini ya kaulimbiu ya “Kiswahili kwa Amani, Mshikamano na Diplomasia ya Uchumi Duniani,” likiwa sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Kiswahili Duniani inayoadhimishwa kila mwaka Julai 7.

Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma 

SERIKALI imesema Kamati za Watu Wenye Ulemavu zilizoanzishwa katika ngazi za Mkoa, Wilaya, Vijiji na Mitaa zinaendelea kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Sheria ya Watu Wenye Ulemavu Na. 9 ya Mwaka 2010, huku utekelezaji wa majukumu hayo ukifikia asilimia 52.

Kauli hiyo imetolewa bungeni na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Dkt Festo Ndugange alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Stella Ikupa Alex, aliyetaka kufahamu kama kamati hizo zinafanya kazi katika maeneo mbalimbali nchini.

Dkt Ndugange amesema sheria imezipa kamati hizo jukumu la kufuatilia upatikanaji wa huduma muhimu kwa watu wenye ulemavu, ikiwemo afya, elimu, ajira, ulinzi wa jamii pamoja na miundombinu jumuishi.

Aidha, kamati hizo zina wajibu wa kushauri Sekretarieti za Mikoa na Halmashauri kuhusu masuala yanayohusu watu wenye ulemavu, kufuatilia utekelezaji wa mipango na bajeti zinazowahusu, pamoja na kupokea na kujadili changamoto zinazowakabili na kupendekeza ufumbuzi wake.

Katika hatua nyingine, Dkt  Ndugange amesema kupitia kamati hizo, jumla ya watu wenye ulemavu 328,733 wametambuliwa nchini kote. Kati yao, wanaume ni 162,464 huku wanawake wakiwa 166,269.

Ameeleza kuwa utambuzi à sasa àhuo umeiwezesha Serikali kupata takwimu sahihi zinazotumika katika upangaji, utekelezaji na ufuatiliaji wa huduma mbalimbali za kijamii kwa watu wenye ulemavu.

Serikali imeahidi kuendelea kusimamia na kuhakikisha kamati hizo zinafanya kazi kwa ufanisi na kwa kuzingatia matakwa ya sheria ili kuimarisha ustawi na ushiriki wa watu wenye ulemavu katika maendeleo ya taifa.


Wananchi wa Jimbo la Kilindi wamepokea kwa furaha taarifa ya Serikali kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya ya sekondari katika Kata ya Msanja, Kijiji cha Muungano Jimbo la Kilindi, Hatua hiyo inalenga kuongeza fursa za elimu kwa vijana pamoja na kuboresha mazingira ya kujifunzia katika eneo hilo.

Mradi huo unatarajiwa kuanza kutekelezwa mara moja na utasaidia kupunguza changamoto ya wanafunzi kusafiri umbali mrefu kufuata huduma za elimu ya sekondari, hali itakayowezesha upatikanaji wa elimu kwa urahisi zaidi kwa wakazi wa Kata ya Msanja na maeneo jirani.

Akizungumza kuhusu maendeleo hayo, Juni 11, 2026, Mbunge wa Jimbo la Kilindi, Mhe. Salehe Mbwana Mhando, ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuwekeza katika sekta ya elimu na kutekeleza miradi ya maendeleo inayogusa maisha ya wananchi moja kwa moja.

Wananchi wa Kata ya Msanja na Jimbo la Kilindi kwa ujumla wameeleza shukrani zao kwa Serikali kwa kuendelea kuwaletea miradi ya maendeleo yenye manufaa kwa jamii, aidha wameahidi kutoa ushirikiano unaohitajika ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati na kwa viwango vinavyostahili.



Waziri wa Mambo ya Nje na Masuala ya Ulaya wa Jamhuri ya Slovakia, Mhe. Juraj Blanár, amewasili nchini kwa ziara ya kikazi kuanzia Juni 10 hadi 11, 2026, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na ushirikiano kati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Slovakia.

Katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) jijini Dar es Salaam Mhe. Juraj Blanár alilakiwa na Naibu Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. James Milya (Mb).

Akiwa nchini, Mhe. Blanár atashiriki katika mazungumzo ya pande mbili na mwenyeji wake, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Dkt. Mahmoud Thabit Kombo (Mb.) yatakayofanyika Juni 11 2026.

Ziara hii inalenga kuimarisha ushirikiano katika sekta mbalimbali ikiwemo utalii, elimu, programu za ufadhili wa masomo, usalama wa mtandao, biashara na uwekezaji.

Baada ya mazungumzo na mwenyeji wake watazungumza na waandishi wa habari na baadaye watashiriki katika hafla ya uzinduzi wa Ubalozi wa Jamhuri ya Slovakia jijini Dar es Salaam. Ubalozi huo ulifunguliwa mwezi Novemba 2025 na unaashiria dhamira ya pamoja ya Tanzania na Slovakia ya kuimarisha zaidi uhusiano wa kidiplomasia pamoja na kupanua maeneo ya ushirikiano wa maendeleo na uchumi.

Waziri Blanár ambaye ameambatana na wafanyabiashara wapatao 50 atashiriki katika Kongamano la Biashara la Tanzania Slovakia litakalokutanisha wafanyabiashara na wawakilishi wa sekta binafsi kutoka nchi zote mbili. 

Kongamano hilo linatarajiwa kujadili fursa za biashara na uwekezaji, kukuza uhamishaji wa teknolojia na kuimarisha ushirikiano katika sekta za kimkakati zikiwemo nishati jadidifu, uchakataji wa mazao ya kilimo na ubunifu wa kidijitali.

















-Ahimiza kuwekeza kwenye miundombinu inayochochea vyanzo vya uwekezaji.

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuondoa vikwazo na kuimarisha ushirikiano na sekta binafsi ili kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini.

Ameyasema hayo leo (Jumatano, Juni 10, 2026), wakati akizindua ghala la forodha la kampuni ya Ciwaye Trading Co. Ltd Wilayani Chamwino mkoani Dodoma.

“Kama tunavyoheshimu sekta ya umma, tunatakiwa kuheshimu sekta binafsi kwa uzito ule ule, kama mataifa mengine yaliyoendelea, uchumi wa mataifa hayo nguzo yake ni sekta binafsi.”

Dkt. Mwigulu aliongeza kwa kusema “Kwa kuheshimu hilo, nimeona nije kuzindua mradi huu, kama ambavyo nimepita kwenye ziara kuzindua miradi ya Serikali, ndiyo maana nimeona na hapa nije mwenyewe.”

Aidha, ameeleza kuwa mradi huo una umuhimu mkubwa katika maendeleo ya nchi, hivyo hauna budi kulelewa.

“Ukubwa wa jambo hili haupimwi kwa majengo, bali kwa uthubutu na matokeo yanayoakisi Dira yetu ya maendeleo na maono ya Rais wetu ya kuhakikisha mradi kama huu unatoa matokeo yaliyokusudiwa.” Amesisitiza Waziri Mkuu Mwigulu.

Waziri Mkuu ameongeza kuwa mradi huo unatazamwa na Serikali kama mradi wa kielelezo wa kutekeleza Dira 2050 na ndiyo maana Serikali imekuwa ikiboresha mazingira ya uwekezaji nchini, ikiwemo maboresho ya sheria za uwekezaji.

“Zimebadilishwa Sheria za uwekezaji ili kuhakikisha wazawa wananufaika na kuushika uchumi, zamani vivutio vya uwekezaji viliwanufaisha wageni, lakini sasa wazawa wanapata vivutio hivyo,” ameeleza Waziri Mkuu.

Ameongeza kuwa: “Mfano katika sekta ya uzalishaji, zamani miradi yote mikubwa ilikuwa inatekelezwa na wageni, lakini mabadiliko hayo ya sheria yamewezesha wazawa kutekeleza miradi mikubwa, na sasa wanaweza kuajiri wageni katika utekelezaji wa miradi hiyo.”

Waziri Mkuu Mwigulu amesema mkakati mwingine unaoenda sambamba na mabadiliko ya sheria, ni pamoja na kuondoa zaidi ya tozo 270 ili kuwapunguzia mzigo wafanyabiashara na walaji wa mwisho.

Akizungumzia utekelezaji wa mradi huo, Waziri Mkuu ameeleza kufurahishwa na hatua zilizofikiwa katika utekelezaji wake, kwani umetekelezwa ndani ya muda mfupi lakini viwango vya ubora vimezingatiwa.

Amesema uamuzi wa kuanzisha ghala hilo mkoani Dodoma ni wa kimkakati kwani Dodoma ipo katikati ya nchi, ikiunganisha maeneo mengine ya nchi na fursa zilizopo katika maeneo hayo, ambapo amewataka wafanyakazi wa mradi huo kuwa waaminifu ili mradi uwe na faida endelevu, kwao binafsi na jamii.

Pia Waziri Mkuu Mwigulu amewahimiza Wakuu wa Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhamasisha wawekezaji kuwekeza kwenye mikoa na maeneo yao kwa kuweka miundombinu inayochochea vyanzo vya mapato na kukua kwa uchumi.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu Mwigulu ameuagiza Wakala wa Barabara za Mijini na Vijini (TARURA) kukaa kwa haraka na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) na kufanya tathmini ya ujenzi wa barabara ya kiwango cha lami ya kilometa 25 kuanzia Chamwino kwenda kituo cha treni cha Igandu ili kusaidia ufanisi wa ghala lililojengwa kwani barabara hiyo itaunufaisha mradi huo.

Kwa upande wake Meneja Masoko wa ghala hilo, Leroy Nelson amesema mradi huo umegharimu zaidi ya shilingi bilioni tatu ambapo utekelezaji wake umekamilika kwa asilimia 100.







Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imeshiriki uzinduzi wa Ghala la Forodha la Kampuni ya Ciwaye lililopo Chamwino mkoani Dodoma, hatua inayolenga kuhamasisha ulipaji wa kodi kwa hiari na kuongeza fursa za uwekezaji wa kibiashara katika mkoa huo.

Akizungumza kwa niaba ya Kamishna Mkuu wa TRA katika hafla hiyo iliyozinduliwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, Naibu Kamishna wa Shughuli za Forodha, Wahabi Matengo, Juni 10, 2026,  amesema ghala hilo ni la kwanza la aina yake katika Mkoa wa Dodoma na lina mchango mkubwa katika kuwezesha biashara halali na kukuza uchumi.

Matengo amesema maghala ya forodha ni nyenzo muhimu inayotolewa kwa mujibu wa Sheria ya Forodha ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya mwaka 2004 iliyofanyiwa marejeo mwaka 2025 pamoja na Kanuni za Forodha za mwaka 2010.

Ameeleza kuwa ghala hilo limeanzishwa kwa ajili ya kuhifadhi magari madogo na makubwa, matrela pamoja na mitambo mbalimbali, huku bidhaa zote zikiwa chini ya usimamizi wa Idara ya Forodha na Ushuru wa Bidhaa hadi zitakapokamilisha taratibu za kiforodha na kulipiwa kodi stahiki.

Akifafanua faida za maghala ya forodha, Matengo amesema mfumo huo hurahisisha ulipaji wa kodi kwa kuwa wafanyabiashara wanaweza kuingiza bidhaa nchini na kuzihifadhi ghalani bila kulipa kodi mara moja, Kodi hulipwa pale bidhaa zinapotolewa kwa matumizi ya ndani ndani ya kipindi kisichozidi mwaka mmoja tangu kuhifadhiwa kwake.

Aidha, amesema maghala hayo yanakuza biashara ya kimataifa kwa kuruhusu bidhaa zilizohifadhiwa kuuzwa ndani na nje ya nchi, sambamba na kuongeza mtiririko wa fedha kwa wafanyabiashara kwani fedha ambazo zingetumika kulipia kodi mara moja hutumika kuimarisha mitaji ya biashara.

Faida nyingine alizozitaja ni pamoja na kuhakikisha upatikanaji wa bidhaa kwa wakati pamoja na kurahisisha matumizi ya misamaha ya kodi kwa wafanyabiashara wanaostahili kwa mujibu wa sheria.

Matengo ameihakikishia Kampuni ya Ciwaye ushirikiano wa karibu kutoka TRA pamoja na utoaji wa miongozo mbalimbali ili kuhakikisha shughuli zote za ghala hilo zinafanyika kwa kuzingatia sheria na kuchangia ukuaji wa mapato ya serikali pamoja na maendeleo ya uchumi wa Mkoa wa Dodoma na Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake, Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba amesema Serikali imeendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuboresha mazingira ya biashara nchini, ikiwemo kupunguza tozo na kufanya marekebisho ya sheria kadhaa ili kuimarisha sekta ya uwekezaji na biashara.

Amesema Serikali inatarajia kuona utekelezaji wa baadhi ya mapendekezo yaliyotolewa na wadau kuanza kuleta matokeo yanayoakisi matarajio ya wananchi, huku lengo kuu likiwa ni kuongeza idadi ya wawekezaji wazawa watakaoshiriki kikamilifu katika kukuza uchumi wa nchi.






Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akisalimiana na Rais wa Kenya Mhe. William Samoei Ruto walipokutana wakati wa mkutano wa Jukwaa la Amani la Oslo 2026 (Oslo Forum 2026) unaofanyika mjini Oslo, Norway, tarehe 10–11 Juni 2026. Mkutano huo wa kimataifa wa kila mwaka unawaleta pamoja wasuluhishi wa migogoro, viongozi wa ngazi za juu, na wataalamu wa amani kutoka zaidi ya nchi 50 duniani. Mwaka huu, Oslo Forum inajadili kauli mbiu yenye uzito wa kipekee: "Gharama ya Vita, Thamani ya Amani" ("The Cost of War, the Price of Peace").

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
MKURUGENZI wa Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP Centre), , amesema mfumo wa Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP) hauna mbadala ikiwa Tanzania inalenga kufikia uchumi wa thamani ya dola trilioni moja ifikapo mwaka 2050.

Kauli hiyo ameitoa kupitia ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa X, kufuatia ziara ya Rais wa Singapore, , pamoja na mhadhara wake katika , ambao umeibua mjadala mpana kuhusu safari ya maendeleo ya Singapore kutoka taifa la kipato cha chini hadi kuwa miongoni mwa nchi zilizoendelea zaidi duniani.

Kafulila amesema kuwa kwa mujibu wa takwimu za Shirika la Fedha Duniani (IMF) za mwaka 2026, Singapore ni miongoni mwa nchi zenye pato kubwa zaidi kwa mtu mmoja mmoja duniani, likifikia zaidi ya dola 107,000 kwa mwaka. Hata hivyo, alibainisha kuwa pamoja na mafanikio hayo makubwa, uchumi wa taifa hilo bado haujafikia dola trilioni moja, ukiwa na thamani ya takribani dola bilioni 659.

Alieleza kuwa mwaka 1995 uchumi wa Singapore ulikuwa karibu sawa na wa Tanzania, ukiwa katika kiwango cha dola bilioni 87, jambo linaloonesha kuwa Tanzania inapaswa kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi kwa kiwango kikubwa zaidi kuliko kilichofikiwa na Singapore ili kutimiza lengo la uchumi wa dola trilioni moja ndani ya kipindi cha miaka 25 ijayo.

“Tunapaswa kubadili namna tunavyofanya kazi, kupanga na kutekeleza miradi ya maendeleo. Hii ndiyo njia pekee ya kufikia malengo makubwa yaliyoainishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050,” amesema Kafulila.

Ameunga mkono kauli ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, , ambaye amekuwa akisisitiza umuhimu wa mageuzi makubwa katika mifumo ya utekelezaji wa maendeleo ili kufanikisha malengo ya muda mrefu ya taifa.

Wakati huo huo, Rais Tharman Shanmugaratnam amezitaka nchi za Afrika kutumia kikamilifu mfumo wa PPP kwa kuruhusu sekta binafsi kuendesha miradi inayoweza kufanywa kwa ufanisi zaidi, huku serikali zikielekeza nguvu na rasilimali zake katika maendeleo ya watu kupitia elimu, afya na ujuzi.

Kwa mujibu wa kiongozi huyo, ubora wa rasilimali watu ndio msingi wa ushindani wa taifa katika uchumi wa dunia, akisisitiza kuwa uwekezaji katika watu ndiyo nguzo muhimu ya maendeleo endelevu.

Kauli za viongozi hao zimekuja wakati Tanzania ikiendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuimarisha ushiriki wa sekta binafsi katika miradi ya maendeleo, hatua inayotajwa kuwa muhimu katika kuongeza uwekezaji, ajira na kasi ya ukuaji wa uchumi wa taifa.


WAKALA Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) imeendelea kusisitiza umuhimu wa ulinzi wa Miliki Ubunifu kupitia ushirikiano na wanawake wa fani za Sayansi, Teknolojia, Uhandisi na Hisabati hatua inayolenga kuongeza uelewa kuhusu haki za Miliki Ubunifu ili kuhakikisha bunifu za watanzania zinalindwa, zinathaminiwa na zinachangia kikamilifu katika maendeleo ya jamii na kutatua changamoto zilizoizunguka jamii kwenye maisha yao ya kila siku.

Hayo yamebainishwa na Ofisa Mtendaji Mkuu wa BRELA, Godfrey Nyaisa alipokuwa akifungua warsha ya Miliki Ubunifu kwa wanawake katika fani za Sayansi, Teknolojia, Uhandisi pamoja na Hisabati (STEM) iliyofanyika katika ukumbi wa Tume ya Ushindani jijini Dar es salaam.

Nyaisa amesema warsha hiyo ni muendelezo wa utekelezaji wa mkakati wa BRELA kuwafikia wabunifu waka kada na fani zote ili kuwaelezea umuhimu wa ulinzi na ubiasharishaji wa bunifu zao.

“Kwa kutambua umuhimu wa fani za Sayansi, Teknolojia, Uhandisi na Hisabati katika uvumbuzi BRELA imeona ni vyema kuandaa warsha hii ili kuwapa ninyi nafasi ya kujifunza masuala ya Miliki Ubunifu pamoja na urasimishaji wa biashara zinazotokana na bunifu mnazozifanya,” amesema Nyaisa.

Awali akimkaribisha Ofisa Mtendaji Mkuu Godfrey Nyaisa, Kaimu Mkurugenzi wa Miliki Ubunifu Bw. Seka Kasera amesema idadi ya wanawake katika fani za Sayansi, Teknolojia, Uandisi na Hisabati kwa sasa imezidi kuongezeka na kwamba warsha hiyo itasaidia wanawake wengi kwenye fani ya Sayansi, Teknolojia, Uhandisi na Hisabati kulinda bunifu zao.

Kwa upande wao baadhi ya washiriki wa warsha hiyo walieleza kuwa warsha hiyo imebadilisha kwa kiasi kikubwa mtazamo wao kuhusu masuala ya Miliki Ubunifu hasa kwenye kulinda kazi ambazo wanabuni kwenye kada yao ya STEM.

“Temekuwa tukitengeneza bunifu mbalimbali na tunaishi nazo, unakuta mwingine hajasajili popote wala kulinda bunifu yake ambayo inamsaidia kutambulika, mtu anaweza akabuni leo na mtu mwingine akaja akabuni kitu kinachofanana na chako na akakisajili na wewe ukakosa mahali pakwenda kulalamika hata kama lilikuwa wazo lako,” alieleza Bi. Tanjana Mgonja.

Warsha hiyo yenye kauli mbiu isemayo ‘Bunifu zetu, Nguvu yetu kwa Maendeleo ya Jamii na Taifa Letu’ imewakutanisha kundi la wanawake wenye fani mbalimbali kutoka idara za Sayansi, Teknolojia, Uhandishi na Hisabati ambapo washiriki walipata fursa ya kujadili mada kuhusu Miliki Ubunifu na kutoa mapendekezo yao namna ya kuboresha bunifu zao.






Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha imetoa mikopo yenye thamani ya Shilingi milioni 991.5 kwa vikundi 51 vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu katika robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2025/2026, hatua inayolenga kuongeza fursa za kiuchumi, kupanua biashara na kupunguza umaskini kwa wananchi.

Mikopo hiyo imetolewa katika hafla iliyofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ambapo jumla ya Shilingi milioni 359 zilitolewa kwa vikundi 17 vya wanawake, Shilingi milioni 557 kwa vikundi 25 vya vijana na Shilingi milioni 75 kwa vikundi tisa vya watu wenye ulemavu.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini, Mhe. Silvestry F. Koka, amesema mikopo ni nyenzo muhimu ya kuwawezesha wananchi kujikwamua kiuchumi, hasa kwa kuzingatia kuwa wengi hukosa mitaji kutokana na masharti magumu ya taasisi za kifedha.

Amesema Halmashauri inapaswa kuendelea kutoa mafunzo ya ujasiriamali na usimamizi wa fedha ili kuhakikisha walengwa wanatumia mikopo hiyo kwa tija na kurejesha kwa wakati.

“Wapo wananchi wenye uwezo wa kufanya biashara lakini wanakosa mtaji kutokana na kutotimiza vigezo vya mikopo ya taasisi za fedha. Kupitia mikopo hii ya Halmashauri tunaendelea kufungua milango ya fursa na kupunguza umaskini kwa wananchi wetu,” alisema Mhe. Koka.

Mbunge huyo amebainisha kuwa zaidi ya Shilingi bilioni 4.5 ziko katika mzunguko wa mikopo iliyotolewa na Halmashauri, hali inayochochea ukuaji wa biashara, kuongeza ajira na kupanua wigo wa mapato ya ndani ya Manispaa.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Mhe. Nickson Simon John, aliwataka wanufaika kuwa na nidhamu ya matumizi ya fedha na kuhakikisha mikopo hiyo inatumika kwa malengo yaliyokusudiwa.

“Fedha ni kama damu katika uchumi. Zinapozunguka kwa usahihi huleta uhai wa biashara, huongeza uzalishaji na kuinua maisha ya wananchi. Ni muhimu mikopo hii ikatumike kwa shughuli za maendeleo badala ya matumizi yasiyo na tija,” alisema.

Awali, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha, Dkt. Rogers Shemwelekwa, amesema kuwa katika mwaka wa fedha 2025/2026 Halmashauri tayari imetoa jumla ya Shilingi bilioni 2.1 kwa vikundi 457 vya makundi maalum.

Amefafanua kuwa kati ya fedha hizo, Shilingi bilioni 1.09 zimetolewa kwa vikundi 275 vya wanawake, Shilingi milioni 904.5 kwa vikundi 161 vya vijana na Shilingi milioni 158.8 kwa vikundi vya watu wenye ulemavu.

Utoaji wa mikopo hiyo unaendelea kuthibitisha dhamira ya Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha ya kutumia mapato ya ndani kuwawezesha wananchi kiuchumi, kuongeza ushiriki wao katika shughuli za uzalishaji na kujenga msingi wa maendeleo jumuishi yanayowanufaisha makundi mbalimbali ya jamii.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Zanzibar inakusudia kuimarisha uhusiano na ushirikiano na Jamhuri ya Singapore kwa kuelekeza nguvu zaidi katika diplomasia ya uchumi, biashara na uwekezaji.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo tarehe 10 Juni, 2026 Ikulu alipofanya mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mhe. Tharman Shanmugaratnam, Ikulu Zanzibar ambapo alizikaribisha kampuni na wawekezaji wa Singapore kuwekeza Zanzibar katika sekta za uchumi wa buluu, utalii, nishati, teknolojia na kuongeza thamani ya mazao ya baharini na mwani.

Kwa upande wake, Rais Tharman Shanmugaratnam amepongeza hatua kubwa za maendeleo zinazofanywa Zanzibar na kuahidi kuhamasisha wawekezaji wa Singapore kuja kuwekeza Zanzibar.

Baada ya mazungumzo hayo, Rais Dkt. Mwinyi, alimwandalia mgeni wake, Rais Tharman dhifa ya chakula cha mchana iliyofanyika Ikulu Zanzibar.









Top News