RAIS Mstaafu Dkt, Jakaya Mrisho Kikwete ameteuliwa kuwa Mwakilishi Maalum wa Umoja wa Afrika kwa Ukanda wa Pembe ya Afrika na Bahari Nyekundu, jukumu linalomrejesha katika mstari wa mbele wa diplomasia ya bara Afrika.

Uteuzi huo ulitangazwa na Mahmoud Ali Youssouf, Mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika, ambaye alionesha imani kubwa katika uzoefu na uongozi wa Kikwete kushughulikia changamoto tata za kisiasa, amani na usalama katika ukanda huo.

Ukanda huo unaendelea kuwa na changamoto nyingi, kuanzia migogoro ya kisiasa hadi maslahi ya kimkakati ya kimataifa, hasa kutokana na umuhimu wa Bahari Nyekundu katika biashara ya dunia. 

Ni eneo ambalo si tu linahusu nchi za Afrika, bali pia lina mvuto wa nguvu za kimataifa.

Katika nafasi hiyo mpya, Kikwete anatarajiwa kusaidia Tume hiyo  kuimarisha juhudi za kuleta amani kupitia diplomasia ya kuzuia migogoro, kukuza mazungumzo jumuishi, na kujenga uaminifu miongoni mwa wadau mbalimbali.

Aidha, alikabidhiwa jukumu la kuratibu juhudi za taasisi mbalimbali, ikiwa ni pamoja na Intergovernmental Authority on Development, East African Community, League of Arab States pamoja na United Nations, ili kuhakikisha juhudi za kuleta amani zinakuwa na mshikamano na ufanisi.

Hili linaonekana kuwa jukumu nyeti zaidi, kwani ukanda huo kwa muda mrefu umekuwa ukivutia maslahi yanayokinzana kutoka kwa mataifa na taasisi mbalimbali. Kuleta mwelekeo mmoja kunahitaji busara, uvumilivu na ustadi wa hali ya juu wa kidiplomasia.

Na wengi wanaamini kwamba  hapo ndipo nguvu ya Dkt. Kikwete ilipo.

Siku zote amejulikana kwa mtindo wa uongozi wa mazungumzo badala ya mabavu, ushawishi badala ya shinikizo. Katika ukanda ambao mara nyingi nguvu za kijeshi hazijaleta suluhu ya kudumu, mtazamo huu unaweza kuwa wa faida kubwa.

Kwa Tanzania, uteuzi huu uliibua hisia za fahari ya kimya. Kwa miaka mingi, nchi imejijengea sifa ya kuwa na mchango mkubwa katika diplomasia ya bara—kuanzia enzi za Mwalimu Nyerere hadi viongozi waliomfuata

Uteuzi wa  Dkt Kikwete umetajwa kuwa ni ukumbusho kwamba uongozi hauishii madarakani. Mara nyingi, viongozi wastaafu hupata nafasi ya kutumia uzoefu wao kwa uhuru zaidi katika jukwaa la kimataifa, na wakati mwingine kwa mafanikio makubwa zaidi.

Mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika alieleza imani yake kwamba hekima na uzoefu wa Kikwete vitachangia kwa kiasi kikubwa katika kutafuta suluhu za kudumu za amani na ustawi katika ukanda huo.

Kwa Pembe ya Afrika, safari bado ni ndefu na yenye changamoto. Lakini diplomasia ni mchakato wa hatua kwa hatua, na si wa matokeo ya haraka. Na kwa kumteua Jakaya Kikwete, Umoja wa Afrika unaonekana kuchagua si tu kiongozi mwenye uzoefu, bali pia mtazamo wa subira, mazungumzo na matumaini ya suluhu ya kudumu.



CHIFU wa Kibondo mkoani Kigoma Mama Mwamvua Rajab Ruhaga Nyamaliza amefariki dunia ghafla asubuhi ya tarehe 24 Machi 2026 akiwa msibani Malinyi, mkoani Morogoro.

Taarifa za kifamilia zinaeleza kuwa marehemu alikuwa amesafiri kwenda Malinyi kuhudhuria mazishi ya binti yake, Zubeda Juma Ruhaga, kabla ya kifo chake hicho cha kushtukiza kutokea.

Kifo hicho kimeacha simanzi kubwa kwa familia, ndugu, jamaa na wakazi wa Kibondo, ambako marehemu alikuwa akihudumu kama kiongozi wa kimila na mshauri muhimu wa jamii.

Kwa sasa, familia ipo katika maandalizi ya kusafirisha mwili wa marehemu kutoka Morogoro kuelekea Kibondo, Kigoma, kwa ajili ya mazishi yatakayofanyika nyumbani kwake.

Taarifa zaidi kuhusu taratibu za mazishi zinatarajiwa kutolewa na familia kadri mipango inavyoendelea.
Na Mwandishi Wetu
WATANZANIA wanatarajiwa kunufaika na huduma za afya za kimataifa kufuatia ushirikiano wa kimkakati kati ya AXA Health International, Alliance Insurance Corporation Limited na MIC Global Risk Tanzania Ltd, hatua inayolenga kupanua upatikanaji wa bima ya afya ya kimataifa pamoja na matibabu maalum nje ya nchi.

Kupitia ushirikiano huo, kampuni hizo tatu zimeunganisha utaalamu wao ili kurahisisha upatikanaji wa huduma za afya za kiwango cha juu kwa watu binafsi, wafanyabiashara, wageni wanaoishi nchini pamoja na wataalamu wanaosafiri kimataifa. Mpango huo unawawezesha wateja kupata matibabu maalum katika hospitali za nje ya nchi pale inapohitajika kupitia bima ya afya ya kimataifa.

Hatua hiyo inakuja kufuatia ushirikiano wa AXA Health International na Executive Healthcare Solutions ulioanzishwa Oktoba 2025 kwa lengo la kuimarisha mfumo wa usambazaji wa huduma za bima ya afya ya kimataifa nchini Kenya na maeneo mengine ya Afrika. Nchini Tanzania, MIC Global Risk Tanzania Ltd imechaguliwa kuwa msambazaji wa kipekee wa huduma hizo katika soko la ndani kwa kushirikiana na Alliance Insurance Corporation Limited.

Kupitia mpango unaojulikana kama Global Executive Health Plan (GEHP), wateja watapata fursa ya kufikia mtandao mpana wa hospitali na wataalamu wa afya wanaotambulika kimataifa, pamoja na huduma za ziada kama uokoaji wa kimatibabu na uratibu wa matibabu yanayofanyika nje ya mipaka ya nchi.

Akizungumzia ushirikiano huo, Afisa Mkuu wa Uendelezaji wa Biashara wa AXA Global Healthcare, Karim Idilby, amesema kuanzishwa kwa huduma hiyo nchini Tanzania ni hatua muhimu katika mkakati wa kampuni hiyo kupanua uwepo wake katika masoko yenye ukuaji wa haraka barani Afrika.

Amesema kadri Tanzania inavyoendelea kuwa kitovu cha uwekezaji, biashara na kubadilishana uzoefu wa kitaalamu, ndivyo mahitaji ya huduma za afya za kimataifa yanavyozidi kuongezeka, jambo linalofanya ushirikiano huo kuwa na umuhimu mkubwa kwa wateja wanaohitaji matibabu maalum nje ya nchi.

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa Alliance Insurance Corporation Limited, Rajiv Kumar, amesema ukuaji wa uchumi wa Tanzania na kuongezeka kwa watu wanaosafiri kimataifa kumeongeza mahitaji ya huduma za afya za kimataifa zilizo salama na zinazoaminika.

Naye Afisa Mtendaji Mkuu wa MIC Global Risk Tanzania Ltd, Aly Maherali, amesema mpango wa GEHP unaunganisha uzoefu wa kimataifa wa AXA Global Healthcare na mfumo wa bima ya ndani unaosimamiwa na Alliance Insurance Corporation Limited, hatua inayowapa watu binafsi, makampuni na wataalamu nchini Tanzania fursa ya kupata ulinzi wa afya katika kiwango cha kimataifa.

Amesema kwa zaidi ya miaka 25 kampuni yake imekuwa mstari wa mbele katika utoaji wa bima ya afya ya kimataifa katika ukanda wa Kusini mwa Jangwa la Sahara, na ushirikiano huo unaimarisha dhamira ya kuendelea kuwahudumia wateja nchini Tanzania na Afrika kwa ujumla.












Matukio mbalimbali katika Picha.

Mkoa wa Mtwara umeendelea kupiga hatua katika kuboresha Sekta ya Elimu kufuatia utekelezaji wa Mradi wa Kuimarisha Elimu ya Sekondari (SEQUIP), unaosimamiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, huku ukifadhiliwa na Benki ya Dunia.

Akizungumza wakati wa ziara ya ufuatiliaji wa pamoja wa utekelezaji wa mradi huo, Mratibu wa Mradi wa SEQUIP kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI, Bw. Richard Makota, alisema shule za Mkoa wa Mtwara zimeonyesha mafanikio makubwa katika utekelezaji wa mradi.

“Matokeo yanaonekana wazi, hasa katika ongezeko la ufaulu wa wanafunzi kwenye masomo ya sayansi na hisabati, pamoja na matumizi ya teknolojia ya kisasa katika ufundishaji,” alisema Bw. Makota.

Alisema kupitia SEQUIP, maboresho makubwa yamefanyika ikiwemo ujenzi wa miundombinu mipya ya shule, upatikanaji wa vifaa vya kisasa vya TEHAMA kama mbao janja (smart boards) na kompyuta, pamoja na utoaji wa vifaa vya maabara na kemikali kwa ajili ya kuimarisha ufundishaji wa masomo ya sayansi, Hatua iliyoongeza ufanisi katika ujifunzaji na ufundishaji, hasa katika masomo ya sayansi na hisabati ambayo yamepewa kipaumbele maalum ndani ya mradi huo.

Alizitaja baadhi ya shule zilizonufaika kuwa ni Shule ya Ufundi Mtwara, Shule Mpya ya Sekondari Mkanaredi, Shule ya Sekondari ya Wasichana Mtwara na Shule ya Sekondari Sabasaba, ambayo pia ni kituo cha wanafunzi waliorejea shuleni baada ya kukatisha masomo kwa sababu mbalimbali.

Aidha, alieleza kuwa mradi huo umeweka mkazo katika kuwasaidia wanafunzi waliorejea shuleni (re-entry students) kwa kuwapatia mazingira rafiki ya kuendelea na masomo yao bila vikwazo, hatua inayolenga kuhakikisha kila mwanafunzi anapata haki ya elimu.

Katika hatua nyingine, serikali imeendelea kuwekeza katika ujenzi wa shule mpya za sekondari ngazi ya kata, ikiwemo shule ya bweni ya wasichana katika Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu na shule ya sekondari ya amali katika Halmashauri ya Mji wa Masasi.


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb), amesema Ushirikiano kati ya Tanzania na Benki ya maendeleo ya Afrika  (AfDB), katika miradi ya kimkakati  unaendelea kuimarika jambo linawezesha nchi kukua kiuchumi.

Ameyasema hayo Machi 25, 2026 alipokuwa anapokea nakala za hati za utambulisho za Mwakilishi Mkazi  mpya wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) nchini Tanzania Bi. Mary Manneko Monyau, katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.

Mhe. Kombo amesema miradi hiyo imejikita zaidi katika sekta za miundombinu, usafirishaji, na nishati ambazo ni uti wa mgongo wa mabadiliko ya kiuchumi nchini. Ameongeza kuwa kwa sasa Benki hiyo inafadhili miradi 27 ikiwemo  Barabara ya Mzunguko wa Nje ya Dodoma, Ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Msalato, Mradi wa Reli ya Kisasa (SGR)  na Mradi wa nyaya za umeme za chini ya bahari unaounganisha visiwa vya Zanzibar, Pemba, na Mafia.

Aidha amempongeza  Bi. Monyau kwa uteuzi wake na kueleza kuwa Serikali ina imani kubwa na uzoefu wake, hususan kutokana na mafanikio aliyoyaonesha alipokuwa Mwakilishi  Mkazi nchini Sudan.

Kwa Upande wake Bi. Monyau amesisitiza kuwa AfDB itajikita zaidi katika kuoanisha mipango yake na Dira ya Maendeleo ya Tanzania 2050 ambapo imepania kuongeza upatikanaji wa mitaji na kusaidia miradi inayoinua uhuru wa kifedha wa Tanzania, huku ikizingatia kukuza ajira kwa vijana na miundombinu wezeshi itakayochochea ukuaji wa viwanda na biashara kanda nzima.















KAMISHINA Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania(TRA) Yusuph Mwenda amesema Mamlaka hiyo tayari imeanza kuchukua hatua kuelekea kuanza kutumika kwa utaratibu mpya wa kuingiza mafuta ya kula Tanzania Bara kutoka Zanzibar.

Akizungumza wakati wa ziara ya Kamati ya Bajeti ya Baraza la Wawakilishi la Zanzibar Machi 24.2026 jijini Dar es Salaam Mwenda amesema miongoni mwa hatua zilizoanza kuchukuliwa ni pamoja na kuunda kamati ndogo ya wataalam inayohusisha Wizara ya Kilimo kupitia Bodi ya Nafaka na Mazao mchanganyiko, maofisa wa Forodha na waagizaji wa mafuta kwaajili ya kuweka utaratibu utakaoanza kutumika kuingiza mafuta hayo hivi karibuni.

Amesema utaratibu huo mpya unalenga kuwezesha biashara ya Mafuta baina ya Tanzania Bara na Zanzibar na kuchangamsha biashara katika Bandari za Bagamoyo, Mbweni na Kunduchi ambazo ndiyo hutumika kuingiza mafuta hayo.

"Tutatoa punguzo kwa mafuta yanayoingia Tanzania Bara kutoka Zanzibar ili kuwawezesha wanaoingiza mafuta hayo kupata faida, Serikali kupata kodi na pia kulinda viwanda vya ndani" amesema Mwenda.

Aidha Kamishna Mwenda amewaonya wafanyabiashara wa bidhaa hiyo watakaojihusisha na magendo baada ya kuanza kutumika kwa utaratibu huo kuwa Serikali haitasita kuwachukuli hatua kwa mujibu wa sheria.

Katika hatua nyingine Kamishna Mkuu amesema TRA itaendelea kutoa elimu ya kodi kwa wananchi wote na kuwezesha biashara baina ya Tanzania Bara na Zanzibar kwa kuhakikisha kila anayestahili kulipa kodi analipa.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti ya Baraza la Wawakilishi la Zanzibar Mhe. Ali Suleiman Ameir imeipongeza TRA kwa uwajibikaji na kuahidi kuwa wataendelea kushirikiana nayo katika kuieleza jamii umuhimu wa kulipa kodi.

Akizungumza katika kikao hicho, Ameir kazi inayofanywa na TRA imekuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya Taifa hususan kwenye utekelezaji wa miradi ya maendeleo hatua ambayo kwa kiasi kikubwa inachochea ukuaji wa uchumi.

Aidha amesema wamefanya ziara hiyo mahususi kwaajili ya kujifunza namna mfumo wa usimamizi wa kodi za ndani (IDRAS) unavyofanya kazi na kuipongeza TRA kwa kuanza kutumia mfumo huo ambao umeweza kuokoa muda wa walipakodi kwa kupata huduma popote walipo huku ukipunguza kwa kiasi kikubwa watumishi wa TRA kuonana na Walipakodi.

Wajumbe wengine wa Kamati ya Bunge ya Baraza la wawakilishi waliohudhuria kikao hicho wamepongeza juhudi za udhibiti wa magendo zinazofanywa na TRA huku wakiahidi kusimamia vizuri matumizi ya kodi zinazokusaywa.




Dodoma, 25 Machi 2025

TanTrade inaongoza mageuzi ya sekta ya biashara nchini Tanzania kupitia Mpango wa CART.IS, unaolenga kuimarisha biashara ya kidijitali kwa urahisi na ufanisi zaidi.

Kupitia ujumuishaji wa mifumo ya taasisi mbalimbali na matumizi ya taratibu zisizohitaji karatasi, CART.IS inapunguza urasimu, inaokoa muda na gharama, na kurahisisha huduma kwa wafanyabiashara.

TanTrade ikiwa ni mdau muhimu wa mpango huu chini ya Mkurugenzi Mkuu Dkt. Latifa Mohamed Khamis, amebainisha kuwa kupitia Mpango huu, Tanzania inaongeza ushindani wake katika soko la kimataifa kwa kutoa huduma za haraka za kisasa na zenye kuaminika.



Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amesema suala la utekelezaji wa mabadiliko na maboresho yaliyofanyika kwenye Sera ya Elimu na Mafunzo, na Mitaalal inahitaji ushirikiano wa hali ya juu miongoni mwa wadau wote wa elimu, taasisi za serikali na zile zisizo za serikali, wazazi na jamii yote kwa ujumla

Makamu wa Rais amesema hayo, wakati akifungua Kongamano la Kimataifa kuhusu maboresho ya sera ya elimu na mitaala nchini, linalofanyika katikaUkumbi wa Maktaba Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Jijini Dar es Salaam.

Ameitaka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kushirikiana na Taasisi za elimu, hususan Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kuendelea kufanya ufuatiliaji na tafiti ili kubaini dosari zozote zinazoweza kukwamisha utekelezaji wa suala hilo ili kubaini na kuibua maeneo yanayohitaji maboresho zaidi kiutendaji.

Makamu wa Rais, amesema suala la utekelezaji wa mabadiliko na maboresho yaliyofanyika kwenye Sera yetu ya Elimu na Mafunzo, na Mitaala kuanzia Elimu ya Awali, Msingi, Sekondari hadi Elimu ya Juu, linataka Watanzania wote kutafsiri vema maono ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan juu ya mfumo wa elimu unaozingatia kutoa ujuzi na maarifa ili kumwezesha mhitimu kumudu mazingira yake, na kumudu ushindani kwenye ulimwengu wa kazi.

Aidha, Makamu wa Rais amesema suala la elimu jumuishi inayozingatia usawa ni miongoni mwa vipaumbele, ambapo Serikali imeweka msisitizo katika uwepo wa vifaa vya kufundishia na kujifunzia pamoja na miundombinu rafiki kwa ajili ya wanafunzi wenye mahitaji maalum. 

Amesema suala hilo linakwenda sambamba na uandaaji wa walimu wenye ujuzi wa elimu maalum ili kufundisha wanafunzi hao.

Kwa upande wake Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Prof. Adolf Mkenda amesema kongamano hilo la kimataifa kuhusu maboresho ya sera naelimu na mitaala ni fursa nzuri ya ushirikishwaji wa watalaam na wachambuzi kuangalia jinsi ambavyo utekelezaji huo unaendelea.

Amesema kongamano hilo litaangazia zaidi namna bora na ufanisi yakutekeleza mageuzi ya elimu nchini.

Awali akitoa Taarifa kuhusu Kongamano hilo, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Prof. William Anangisye amesema malengo ya kongamano hilo ni kutafakari na kujenga uelewa wa pamoja miongoni mwa wadau mbalimbali kuhusu sera ya sasa ya elimu na mafunzo na marekebisho ya mitaala na athari zake kwa maendeleo endelevu.

Pia, amesema lengo lingine ni kuibua mijadala ya kitaaluma kuhusu mitaala yaelimu ya msingi, sekondari na elimu ya juu, kutafakari juu ya maendeleo yakitaaluma na nafasi ya elimu ya ualimu kulingana na maboresho ya sera yaelimu na mafunzo, kubadilishana uzoefu wa kimataifa na kikanda jinsimaboresho ya elimu yanavyoweza kuchangia ukuaji jumuishi na mustakbaliwa maendeleo endelevu.

Maboresho yaliyofanywa na serikali kwenye baadhi ya maeneo ya Sera ya Elimu na Mafunzo, yamefanyika ili kuondoa changamoto mbalimbali zilizokuwa zikiikabili elimu ya Tanzania, zikiwemo, kujikita zaidi kwenye elimu ya nadharia badala ya vitendo na pia, kutokuwepo kwa fursa za elimu na mafunzo zinazozingatia mahitaji ya soko la ajira. 

Vilevile, mapungufu katika njia za ujifunzaji ambazo hazikukidhi hali halisi ya mazingira na maadili ya Kitanzania.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akizindua Jarida Maalum la Elimu (Papers in Education and Development) wakati wa Kongamano la Kimataifa kuhusu maboresho ya Sera ya Elimu na Mitaala nchini, linalofanyika katika Ukumbi wa Maktaba wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Tarehe 25 Machi 2026.


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akihutubia wakati wa Ufunguzi wa Kongamano la Kimataifa kuhusu maboresho ya Sera ya Elimu na Mitaala nchini, linalofanyika katika Ukumbi wa Maktaba wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Tarehe 25 Machi 2026.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Prof. Adolf Mkenda akizungumza wakati wa Ufunguzi wa Kongamano la Kimataifa kuhusu maboresho ya Sera ya Elimu na Mitaala nchini, linalofanyika katika Ukumbi wa Maktaba wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Tarehe 25 Machi 2026.

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Prof. William Anangisye akizungumza wakati wa Ufunguzi wa Kongamano la Kimataifa kuhusu maboresho ya Sera ya Elimu na Mitaala nchini, linalofanyika katika Ukumbi wa Maktaba wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Tarehe 25 Machi 2026.





Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM), Dkt. Maulid J. Maulid, amefanya kikao kazi na watumishi wa taasisi hiyo kutoka kampasi zote, akisisitiza umuhimu wa uwajibikaji, umoja na mshikamano katika kufanikisha malengo ya taasisi.

Akifungua kikao hicho, Dkt. Maulid mesema kuwa watumishi wanapaswa kuwajibika kikamilifu katika nafasi zao huku wakidumisha mshikamano ili kuongeza ufanisi na tija katika utekelezaji wa majukumu ya taasisi.

“Tunapaswa kuwajibika kwa nafasi zetu kwa kuwa wamoja na wenye mshikamano ili kuleta tija katika utimizaji wa malengo ya taasisi,” amesema Dkt. Maulid.

Katika kikao hicho, watumishi wapya waliojiunga na ADEM kutoka taasisi mbalimbali walipata fursa ya kujitambulisha, ambapo waliaswa kufanya kazi kwa weledi, uadilifu na kujituma ili kuchangia maendeleo ya taasisi hiyo.

Kwa upande wake, Dkt. Lucas Mzelelela amesisitiza umuhimu wa watumishi kuzingatia maadili ya utumishi wa umma kwa kufanya kazi kwa bidii na nidhamu wakati wote wawapo kazini.

“Kila mtumishi anapaswa kutumikia kiapo chake cha utumishi wa umma kwa kuwajibika ipasavyo na kuwa na nidhamu ya kazi kwa muda wote wawapo kazini,” amesema Dkt. Mzelelela.

Kikao hicho kililenga kufanya mapitio ya mipango ya taasisi kwa mwaka wa fedha unaoendelea, kukumbushana majukumu ya kazi pamoja na kusikiliza na kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili watumishi na taasisi kwa ujumla.















Top News