Na Belinda Joseph-Tanga
Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) umewataka wabunifu nchini kusajili bunifu zao mapema ili kulinda haki zao na kuzuia bunifu hizo kutumiwa au kuendelezwa na watu wengine bila ridhaa yao.
Akizungumza Agosti 18, 2026, katika Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu Kitaifa inayoendelea mkoani Tanga, Msajili Msaidizi Mwandamizi kutoka Kurugenzi ya Miliki Ubunifu, Sehemu ya Hataza BRELA, Bi. Neema Kitala, amesema ushiriki wa BRELA katika wiki hiyo unalenga kuwapatia wabunifu elimu kuhusu umuhimu wa kusajili na kulinda bunifu zao.
Kitala amesema Hataza ni haki ya kisheria inayotolewa kwa mbunifu kwa ajili ya kulinda uvumbuzi wake na kumpa mbunifu haki ya kutambuliwa na kunufaika na ubunifu huo.
Amesema bado kuna wabunifu wengi ambao hawajasajili bunifu zao kutokana na kutofahamu taratibu na umuhimu wa usajili, hivyo BRELA inaendelea kutoa elimu katika maeneo mbalimbali nchini.
“Tunawahamasisha wabunifu wote, hasa vijana, kuhakikisha wanasajili bunifu zao mapema ili ziweze kulindwa na kutambuliwa kisheria, wanaweza kutembelea tovuti ya BRELA au kufika moja kwa moja katika ofisi zetu kujisajili".
Amesema usajili ni muhimu kwa sababu mbunifu anapoweka wazi bunifu yake bila kuilinda hususani katika maonesho kama hayo, kuna uwezekano wa mtu mwingine kuitumia, kuendeleza au kutengeneza bidhaa inayofanana na hiyo bila ridhaa ya mbunifu mwenyewe.
Aidha, Kitala amesema BRELA imeendelea kuwafikia wabunifu kutoka maeneo mbalimbali, wakiwemo wanafunzi na wabunifu kutoka vijijini, kwa kuwapatia elimu kuhusu namna ya kusajili bunifu zao na kuzifanya kuwa mali inayotambulika kisheria.
Amesema changamoto kubwa inayowakabili baadhi ya wabunifu ni kudhani usajili wa bunifu zao ni kiasi kikubwa cha fedha, huku akieleza gharama za usajili wa kazi zao BRELA kupitia Hataza ni shilingi elfu 12 kwa sasa ambayo ni kiasi cha kawaida, ametoa rai kwa wabunifu kuanza mchakato wa usajili badala ya kusubiri hadi bunifu zao zitumiwe na watu wengine.
Amesisitiza kuwa kulinda bunifu kupitia hataza ni hatua muhimu kwa mbunifu kwa kuwa kunasaidia kutambua umiliki wa uvumbuzi na kumpa fursa ya kunufaika na kazi yake, huku akiwataka wabunifu kutumia fursa za elimu zinazotolewa na BRELA kupata uelewa zaidi kuhusu usajili na ulinzi wa bunifu zao.





.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)






.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)

.jpeg)































