
.jpeg)

Na Janeth Raphael – MichuziTv
MFUKO wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) umeweka mkakati wa kuhakikisha kaya zitakazonufaika na Mpango wa Tatu wa TASAF zinatumia fursa zitakazotolewa kujijengea uwezo wa kiuchumi na hatimaye kuondokana na utegemezi ndani ya kipindi cha miaka mitatu kabla ya kuhitimu kwenye mpango huo.
Mpango huo unatekelezwa kwa kipindi cha miaka minne, kuanzia mwaka 2026 hadi 2030, ukiwa na lengo la kubadilisha maisha ya kaya maskini kwa kuzipatia fursa za kuongeza kipato, kuimarisha uwezo wa kujitegemea na kujenga msingi wa maendeleo endelevu, badala ya kuendelea kutegemea msaada kwa muda usio na ukomo.
Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF, Shadrack Mziray, amesema hayo wakati wa ziara ya Kamati ya Baraza la Wawakilishi inayosimamia Ofisi za Viongozi Wakuu wa Kitaifa Zanzibar, iliyotembelea Makao Makuu ya TASAF jijini Dodoma.
Mziray amesema mkakati huo unalenga kuhakikisha kaya zinazonufaika na mpango zinatumia ipasavyo fursa zinazotolewa katika kipindi cha miaka mitatu, kabla ya kuhitimu na kuendelea na maisha ya kujitegemea kiuchumi.
Amesema baada ya kaya kuhitimu, TASAF itaendelea kuzifuatilia ili kutathmini maendeleo yake na kuhakikisha zinabaki katika hali ya kujitegemea kiuchumi.
“Lengo letu ni kuona kaya zinatumia fursa hii kama daraja la kutoka kwenye utegemezi na kujenga uwezo wa kujitegemea. Tunataka wanufaika waweze kuongeza kipato na kuboresha maisha yao kwa njia endelevu,” amesema Mziray.
Kwa upande wa mmoja wa wajumbe wa Kamati hiyo ameishauri TASAF kuendelea kuimarisha mifumo ya ufuatiliaji na tathmini ya utekelezaji wa Mpango wa Tatu, ili kuhakikisha malengo yaliyowekwa yanafikiwa na kaya zinazonufaika zinapata matokeo yaliyokusudiwa.
Wajumbe hao wameeleza kuwa ufuatiliaji wa karibu ni muhimu katika kuhakikisha fursa zinazotolewa kwa kaya maskini zinatumika ipasavyo na kuleta mabadiliko ya kiuchumi na kijamii kwa wanufaika.
Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Machano Othman Said, amepongeza TASAF kwa mchango wake katika juhudi za kupunguza umaskini nchini, akisema programu hiyo imeendelea kuwa chachu ya kuwapatia wananchi wa Tanzania Bara na Zanzibar fursa za kuboresha maisha yao.
Machano amesema juhudi za TASAF zimekuwa muhimu katika kuwawezesha wananchi wenye uhitaji kupata fursa zinazowasaidia kuongeza kipato na kujenga uwezo wa kukabiliana na changamoto za kiuchumi.
Utekelezaji wa Mpango wa Tatu wa TASAF unatarajiwa kugharimu zaidi ya Dola za Marekani milioni 650 na unalenga kunufaisha zaidi ya kaya milioni 1.5 zenye uhitaji Tanzania Bara na Zanzibar.
Kupitia mpango huo, TASAF inalenga kuhakikisha uwekezaji unaofanyika kwa kaya maskini hauishii katika kutoa msaada wa muda mfupi, bali unatumika kama msingi wa kuwawezesha wanufaika kuongeza kipato, kujenga uwezo wa kiuchumi na hatimaye kuondokana na utegemezi.
Katibu wa NEC, Uchumi na Fedha wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Jamal Kassim Ali, amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Uchumi Tanzania (TISEZA), Ndugu Gilead John Teri, kuhusu fursa za kimkakati za uwekezaji na namna ya kuongeza mchango wa sekta binafsi katika kukuza uchumi wa Taifa.
Mazungumzo hayo yaliyofanyika katika Ofisi Ndogo za CCM, Lumumba, Dar es Salaam, yalijikita katika maeneo yenye kuchochea ukuaji wa uchumi na kuongeza mapato, ikiwemo uchukuzi na usafirishaji, madini, ardhi na majengo (real estate), pamoja na uwekezaji katika maeneo yenye fursa za kiuchumi.
Pande hizo pia zilijadili namna CCM inavyoweza kuendelea kuendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na kutekeleza kwa ufanisi vipaumbele vilivyoainishwa katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2025–2030, hususan katika kukuza uwekezaji, uzalishaji, ajira na mapato.
Akizungumza katika kikao hicho, Ndugu Jamal alisisitiza umuhimu wa Chama kuwa na mtazamo wa muda mrefu katika kutambua na kutumia fursa za uwekezaji zilizopo nchini.
Alisema ushirikiano kati ya Chama, taasisi za Serikali, wawekezaji na sekta binafsi ni muhimu katika kuhakikisha fursa zilizopo zinabadilishwa kuwa shughuli halisi za kiuchumi zenye tija na manufaa kwa Taifa.
Mazungumzo hayo ni sehemu ya juhudi za CCM za kuimarisha ushirikiano na wadau wa uchumi na uwekezaji, kwa lengo la kuongeza ufanisi, mapato na mchango wa rasilimali za Chama katika maendeleo ya Taifa.
Naibu Katibu Mkuu CCM Zanzibar, Ndg. Abdi Mahamoud Abdi, amewataka viongozi na watendaji wa chama katika ngazi zote kufanya kazi kwa bidii, mshikamano na ushirikiano wa pamoja ili kuhakikisha Chama Cha Mapinduzi kinaendelea kupata matokeo chanya katika utekelezaji wa majukumu yake.
Ndg. Abdi ameyasema hayo leo, Agosti 17, 2026, katika ukumbi wa Jengo la Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui, Zanzibar, wakati akizungumza katika kikao cha pamoja kilichowakutanisha viongozi na watendaji wa CCM, Jumuiya ya Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), Jumuiya ya Wazazi pamoja na watendaji wa Afisi Kuu ya CCM Zanzibar.
Amesema kila mtendaji wa chama ana jukumu la kuhakikisha anatekeleza majukumu yake kwa bidii, uadilifu na kwa kuzingatia wajibu aliopewa katika kitengo chake, huku akisisitiza umuhimu wa kudumisha ushirikiano na watendaji wenzake.
Ndg. Abdi amesema mafanikio ya chama yanategemea kwa kiasi kikubwa namna viongozi na watendaji wake wanavyoshirikiana katika kutekeleza majukumu yao, hivyo amewataka kuacha kufanya kazi kwa misingi ya mtu mmoja mmoja na badala yake kujenga utamaduni wa kufanya kazi kwa pamoja.
Aidha, Naibu Katibu Mkuu huyo amewatoa hofu watendaji wa chama kuhusu masuala ya maslahi yao, akisisitiza kuwa ataendelea kusimamia kikamilifu maslahi yao ili kuwawezesha kuwa na mazingira bora yatakayowapa motisha ya kufanya kazi kwa bidii na kwa ufanisi zaidi.
Amesisitiza kuwa watendaji wanapaswa kutumia nafasi zao kwa kutekeleza majukumu ya chama kwa ufanisi, huku wakilinda umoja, mshikamano na misingi ya Chama Cha Mapinduzi.
.jpeg)
Na Mwandishi Wetu
SERIKALI imeombwa kuzipa nafasi kampuni zenye uwezo wa kuzalisha gesi ya Okseji ambayo inajukulikana kwa jina la hewa tiba kwa ajili ya matumizi ya hospitalini kwa kuwa kampuni hizo zinauwezo mkubwa na zimebobea katika uzalishaji huo.
Ombi hilo limetolewa leo jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya TOL Gases PLC Daniel Warungu alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari baada ya kumalizika kwa Mkutano Mkuu wa 31 wa mwaka wa Wanahisa huku akisisitiza wao wamekuwa na uwezo mkubwa wa kuzalisha.
Amesema kwa sekta binafsi zinazalisha gesi ya Oksijeni hivyo ni vema Serikali ikawa inanunua badala ya kuzalisha na kupikia mitambo huku akifafanua anaamini serikali itakubali ombi hilo kwa kuwa imeonesha nia huku akisisitiza uwepo wa nyenzo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 imeonesha jinsi ambavyo sekta binafsi zinavyoweza kuwa mshirika katika utekelezaji wa dira na wao TOL Gases wako tayari.
“Tunafanya uwekezaji mkubwa unaowezesha kuzalisha gesi ya oksijeni kwa ajili ya kuhakikisha kunakuwa na hewa tiba kwa ajili ya mahospitalini hivyo ombi letu Serikali badala ya nayo kuwa inazalisha iweke utaratibu wa kuwa inanunua kutoka sekta binafsi.TOL Gases tunao uwezo mkubwa na tumebobea katika uzalishaji wa oksijeni.”
Kuhusu mkutano wa wanahisa Warungu amesema wamejadili masuala mbalimbali huku akieleza kwa upande wa mapato ya kampuni yaliongezeka kutoka Shilingi bilioni 30.2 mwaka 2024 hadi Shilingi bilioni 31.15 mwaka 2025.
Amefafanua faida kabla ya riba, kodi, uchakavu na punguzo la thamani (EBITDA) iliongezeka kutoka Shilingi bilioni 10.5 hadi Shilingi bilioni 13.4, huku faida kabla ya kodi ikiongezeka kutoka Shilingi bilioni 3.98 hadi Shilingi bilioni 6.78.”Faida baada ya kodi ilifikia Shilingi bilioni 3.98 mwaka 2025, ikilinganishwa na Shilingi bilioni 2.06 mwaka 2024.”
Ameongeza TOL Gases inaendelea kuongeza uwezo wake wa uzalishaji kupitia miradi miwili mikubwa. Miongoni mwa miradi hiyo ni ujenzi wa kiwanda cha Ikama III cha kuzalisha hewa ya ukaa (Carbon Dioxide), kinachotarajiwa kuanza uzalishaji Septemba 2027. Mradi huo utaongeza uwezo wa uzalishaji na kuimarisha upatikanaji wa gesi hiyo.
Aidha kampuni pia inajenga kituo kipya cha kutenganisha hewa (Air Separation Unit – ASU) kwa msaada wa Clinton Health Access Initiative (CHAI). Kituo hicho kinatarajiwa kuanza kufanya kazi Oktoba 2026 na kitaongeza uwezo wa uzalishaji wa oksijeni hadi takribani tani 20 kwa siku, sambamba na kituo kilichoanza kufanya kazi mwaka 2021.
Warungu amesisitiza uwekezaji huo utasaidia kuongeza ufanisi wa uzalishaji, kurahisisha matengenezo ya mitambo bila kuathiri kwa kiasi kikubwa uzalishaji na kuongeza uwezo wa kukidhi mahitaji ya gesi katika sekta ya afya, viwanda na uzalishaji.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Kampuni hiyo Leonard Kitoka amesema Tanzania kwa sasa ina uwezo wa kutosha kutoka kwa wazalishaji binafsi kukidhi mahitaji ya sasa na yajayo ya oksijeni ya tiba, hasa kutokana na uwekezaji mkubwa uliofanywa hivi karibuni katika mitambo ya uzalishaji.
Akizungumza kuhusu Soko la hisa,amesema thamani ya hisa za TOL Gases katika Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) imeongezeka kutoka Shilingi 795 wakati wa Mkutano Mkuu wa Mwaka uliopita hadi kufikia kiwango cha juu cha Shilingi 1,490, sawa na ongezeko la takribani asilimia 74. Kwa sasa, hisa hizo zinauzwa kati ya Shilingi 1,320 na Shilingi 1,490.
“TOL Gases imeeleza kuwa rasilimali za umma zinaweza kutumika kwa ufanisi zaidi katika kuongeza mahitaji na upatikanaji wa oksijeni ya tiba badala ya kuwekeza katika kuongeza zaidi uwezo wa uzalishaji.
“Kampuni inapendekeza hospitali na vituo vya afya kuwezeshwa kununua oksijeni yenye ubora unaohakikishwa kutoka kwa wazalishaji binafsi waliopo, hatua ambayo kwa mujibu wa kampuni itasaidia kutumia kikamilifu uwezo wa uzalishaji uliopo nchini, kuepusha uwekezaji unaojirudia na kuhakikisha upatikanaji endelevu wa oksijeni kwa gharama nafuu.”
Amesisitiza TOL Gases itaendelea kushirikiana na Serikali, taasisi za afya na wadau wa maendeleo kuhakikisha upatikanaji wa oksijeni salama na yenye ubora kwa matumizi ya tiba nchini Tanzania, huku ikiendelea kuwekeza katika uzalishaji, usambazaji na utaalamu wa kiufundi.
Pamoja na hayo amesema kutokana na mikakati ya kampuni hiyo wanahisa kwa kauli moja wamekubaliana kutogawana gawio la faida na badala yake fedha hizo za gawio zitumike katika kuwekeza katika Ujenzi wa miundombinu kwanza ili kuongeza mapato ya kampuni.
.jpeg)
Na Mwandishi Wetu
MAMLAKA ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imeteketeza hekari 3,117.9 za mashamba ya bangi na kukamata watuhumiwa 12 katika operesheni maalum ya siku 16 iliyofanyika katika vijiji vinne vya Kata ya Kandawale na Kipatimo, Wilaya ya Kilwa, mkoani Lindi.
Akizungumza kuhusu operesheni hiyo, Kamishna Jenerali wa DCEA, Aretas Lyimo, amesema mafanikio hayo yametokana na ushirikiano mkubwa kati ya Mamlaka, wananchi na viongozi wa maeneo husika katika mapambano dhidi ya kilimo cha bangi.
Amesema operesheni hiyo ni sehemu ya mkakati endelevu wa DCEA wa kudhibiti uzalishaji wa dawa za kulevya nchini hususan bangi, ambayo imeendelea kulimwa katika baadhi ya maeneo nchini.
"Tumebaini uwepo wa mashamba makubwa ya bangi yaliyolimwa katika ardhi zinazomilikiwa na vijiji na vitongoji. Licha ya serikali kuweka mkakati wa matumizi ya ardhi iliyopo chini ya vijiji na vitongoji lakini bado wananchi wanaitumia ardhi hiyo kulima bangi" amesema Lyimo.
Ameeleza kuwa, kati ya wananchi 200 hadi 250 walishiriki kila siku katika kufyeka mashamba hayo, jambo linalodhihirisha umuhimu wa ushiriki wa jamii katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya.
Aidha, ametoa wito kwa wananchi wote wenye mashamba ya bangi au wanaofahamu uwepo wa mashamba hayo katika maeneo yao nchini kuyateketeza mara moja kabla ya hatua za kisheria kuchukuliwa. Vilevile, amewataka viongozi wa vijiji na kata kuhakikisha wanazuia na kutokomeza kilimo cha bangi katika maeneo yao.
Vilevile, amewataka wasimamizi wa hifadhi za taifa na maeneo mengine ya uhifadhi kuhakikisha maeneo wanayosimamia hayatumiki kulima bangi, akisisitiza kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya yeyote atakayebainika kuruhusu au kushindwa kudhibiti shughuli hizo.
Kwa upande wao, wananchi wa Kijiji cha Nandete, Veronica Mandai na Nassoro Mbonde, wamelaani vikali uwepo wa kilimo cha bangi katika maeneo yao, wakisema kuwa hakina manufaa kwa jamii na kimekuwa kikihatarisha mustakabali wa vijana.
Wamesema wakati mwingine watoto wao hujihusisha na kilimo hicho bila wazazi kufahamu, ndiyo sababu wamejitokeza kwa wingi kushiriki katika zoezi la kuteketeza mashamba ya bangi ili kuonyesha msimamo wao wa kupinga kilimo hicho.
"Nawaomba vijana na wanawake wawe mstari wa mbele kukataa na kutokomeza dawa za kulevya kwa sababu zina madhara makubwa kwa afya na maendeleo ya jamii. Vijana ndiyo nguvu kazi ya taifa na wanawajibu wa kulijenga Taifa. Wakijiingiza katika matumizi au uzalishaji wa dawa za kulevya, watapoteza fursa hiyo na kuathiri maendeleo ya taifa. Vilevile, watoto wanaokulia katika mazingira yanayohusisha dawa za kulevya wako katika hatari ya kupoteza mwelekeo wa maisha yao," amesema Veronica.
Naye Afisa Mtendaji wa Kata ya Kandawale, Mohamed Mpame, amesema baada ya operesheni hiyo viongozi wa kata kwa kushirikiana na vijiji na vitongoji wataimarisha ulinzi na usimamizi wa maeneo yao ili kuhakikisha kilimo cha bangi hakiendelei.
"Tutahakikisha tunafanya doria za mara kwa mara na kuendelea kutoa elimu kwa wananchi ili waachane kabisa na kilimo cha bangi ili mwisho wa siku likitokea la kutokea iwe ni juu yao. Nawashauri watu kutumia ardhi yao kulima mazao ya korosho na kuachana na mazao ya bangi” amesema Mpame.
DCEA itaendelea kufanya operesheni nchi nzima kwa kushirikiana na wananchi na wadau mbalimbali ili kubaini na kutokomeza maeneo yote yanayotumika kwa kilimo cha bangi na kuhakikisha hatua stahiki zinachukuliwa kwa mujibu wa sheria.
NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo,akizungumza wakati wa Mkutano wa Kati ya Wizara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo,akizungumza wakati wa Mkutano wa Kati ya Wizara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Balozi Waziri Salum,akizungumza wakati wa Mkutano wa Kati ya Wizara ya Viwanda na Biashara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), Godfrey Nyaisa,akizungumza wakati wa Mkutano wa Kati ya Wizara ya Viwanda na Biashara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

SEHEMU ya washiriki wakimsikiliza Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo (hayupo pichani) ,akizungumza wakati wa Mkutano wa Kati ya Wizara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

SEHEMU ya washiriki wakimsikiliza Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo (hayupo pichani) ,akizungumza wakati wa Mkutano wa Kati ya Wizara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo,akiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kugungua Mkutano wa Kati ya Wizara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo,akiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kugungua Mkutano wa Kati ya Wizara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo,akiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kugungua Mkutano wa Kati ya Wizara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.
............
NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo, amewataka Maafisa Biashara nchini kutumia nafasi zao kikamilifu kuibua fursa za uwekezaji, kuongeza thamani ya mazao na kuboresha mazingira ya biashara katika halmashauri, hatua inayolenga kuchochea maendeleo ya kiuchumi na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Londo ametoa kauli hiyo leo Agosti 17,2026 jijini Dodoma wakati wa Kikao cha Tatu cha Wizara ya Viwanda na Biashara na Maafisa Biashara nchini, kilicholenga kuimarisha utekelezaji wa majukumu yao katika kukuza biashara, viwanda na uwekezaji.
Amesema Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inalenga kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha uchumi wa viwanda katika Afrika Mashariki na Kati, ikiwamo kufikia uchumi wa dola trilioni moja na kuongeza kipato cha Mtanzania hadi dola 7,000. Amesema kufikia malengo hayo kunahitaji uchumi imara, jumuishi na shindani unaotegemea sekta binafsi, sayansi na teknolojia, uwekezaji, utafiti pamoja na nguvu kazi yenye ujuzi.
"Maafisa Biashara wana jukumu la kuhakikisha halmashauri zinakuwa vituo vya uzalishaji, uwekezaji na biashara kwa kutambua fursa zilizopo, kuwaunganisha wazalishaji na masoko na kuhakikisha mazao yanaongezwa thamani. "amesema Mhe.Londo
Hata hivyo ametolea mfano wa mahindi, amesema wakulima wanapaswa kusaidiwa kuondokana na kuuza mazao ghafi na badala yake kuzalisha bidhaa kama unga wenye chapa na kuufikisha kwenye masoko, hatua itakayoongeza kipato na kuchangia kupunguza umaskini.
Aidha, amesema utekelezaji wa Dira 2050 unahitaji vijana, wanawake na watu wenye ulemavu kushirikishwa kikamilifu katika uzalishaji, uwekezaji na biashara kupitia fursa za mikopo na uwezeshaji. Amesema katika mwaka wa fedha 2025/2026, viwanda vikubwa vipya 25 vilijengwa katika sekta mbalimbali na kutoa ajira 39,000, zikiwamo ajira 7,600 za moja kwa moja na 31,000 zisizo za moja kwa moja.
Katika kuimarisha mazingira ya uwekezaji, Londo amezitaka mikoa kuhuisha kanzidata za viwanda, biashara, masoko, leseni, wawekezaji na maeneo yaliyotengwa kwa shughuli za kiuchumi, huku kila halmashauri ikiandaa wasifu wa fursa za uwekezaji unaoonyesha upatikanaji wa malighafi, miundombinu, masoko na maeneo ya uwekezaji. Pia amewataka Maafisa Biashara kuhakikisha Mabaraza ya Biashara yanafanya kazi kikamilifu na hoja za sekta binafsi zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati.
Katika hatua nyingine, Londo amewataka Maafisa Biashara kuharakisha urasimishaji wa biashara zisizo rasmi kwa kutoa elimu kuhusu usajili wa biashara, leseni, TIN, viwango, vipimo na taarifa za umiliki.
Amesema urasimishaji utawawezesha wafanyabiashara kupata huduma za uwezeshaji, mitaji na masoko, huku akieleza kuwa halmashauri zimetengewa asilimia tano ya mapato ya ndani, yenye thamani ya zaidi ya Sh bilioni 72 kwa mwaka wa fedha 2026/2027, kwa ajili ya kuwekeza katika miundombinu ya masoko, maeneo ya biashara na ujasiriamali.
Amesisitiza fedha hizo zitumike kwa ufanisi kwa kushirikisha sekta za ardhi, maji, nishati na barabara ili kuongeza tija kwa wafanyabiashara na kuvutia wawekezaji. Aidha, amewataka Maafisa Biashara kutumia nafasi zao kuboresha huduma na kuifanya Tanzania kuwa na mazingira bora zaidi ya biashara na uwekezaji, hatua ambayo ni muhimu katika kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Balozi Waziri Salum, amewataka Maafisa Biashara kuongeza udhibiti wa bidhaa feki na viwanda visivyo rasmi katika maeneo yao, akieleza kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kulinda afya na usalama wa wananchi, watumiaji pamoja na wazalishaji wanaofuata sheria.
Naye Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), Godfrey Nyaisa, amesema Maafisa Biashara ni kiungo muhimu kati ya Serikali na wafanyabiashara katika kuhakikisha sera, sheria na kanuni za biashara zinatekelezwa na kuleta mabadiliko chanya katika mazingira ya biashara na uwekezaji nchini.
Amesema kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, BRELA imeendelea kuboresha mifumo na sheria zinazosimamia usajili na utoaji wa leseni kwa lengo la kupunguza muda na gharama za kuanzisha na kuendesha biashara. Amesema kupitia BRELA Online System (ORS), huduma za wakala zimeunganishwa katika mfumo mmoja, huku mfumo huo ukiwezesha pia utoaji na usimamizi wa leseni za biashara kundi A na B.
Amesema mfumo huo unatoa fursa kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa kutoa na kusimamia leseni za kundi B bila kuathiri mapato yao, kwani malipo yanayofanywa na mfanyabiashara yanaingia moja kwa moja katika akaunti ya halmashauri husika.
Aidha, ORS imeunganishwa na mifumo ya taasisi nyingine za Serikali ikiwamo NIDA na TRA, hatua inayowezesha taarifa muhimu kupatikana moja kwa moja bila mfanyabiashara kuwasilisha nyaraka ambazo tayari zipo kwenye mifumo hiyo.
Nyaisa,amesema kuwa maboresho hayo yameongeza uwazi na ufanisi, kupunguza urudufu wa taarifa, muda na gharama za kupata huduma, pamoja na kupunguza mianya ya uzembe katika utoaji wa huduma.
"BRELA itaendelea kushirikiana na Wizara ya Viwanda na Biashara, Ofisi ya Waziri Mkuu–TAMISEMI, sekretarieti za mikoa na halmashauri katika kuwajengea uwezo Maafisa Biashara."amesema Nyaisa
Amesema katika mwaka wa fedha 2026/2027, BRELA imepanga kutoa mafunzo kwa Maafisa Biashara wote nchini kupitia kanda nne, yatakayolenga matumizi ya mifumo, utoaji na usimamizi wa leseni pamoja na utekelezaji wa sheria.
Pia amesema BRELA itaendelea kuboresha miunganiko ya mifumo ya kidijitali na kushirikiana na vyama vya Maafisa Biashara katika kutatua changamoto zao, huku akisisitiza kuwa maafisa hao ni mawakala muhimu wa uwekezaji nchini na wanapaswa kutambua kuwa jukumu lao ni kuwezesha biashara, si kuikwamisha, ili kujenga mazingira rafiki kwa wafanyabiashara na wawekezaji.










.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)







.jpeg)



.jpeg)
.jpeg)





.jpeg)


.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
