Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu amesema Serikali itaendelea kushirikiana na Taasisi za Dini nchini kuimarisha maadili kwa jamii na kukuza maemdeleo.

Mhe. Sangu amesema hayo alipomwakilisha Waziri Mkuu Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba katika hafla ya kumsimika uaskofu mchungaji Daniely Liyaseke wa Kanisa la The Charismatic Episcopal Church of Tanzania, Dayosisi mpya ya Ukanda wa Tanzanite One, iliyofanyika Mei 31, 2026 Kijiji cha Terat, Wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Sangu amesema Serikali inatambua na kuthamini mchango wa makanisa katika kuimarisha maadili, mshikamano wa kijamii na maendeleo ya Taifa na itaendeleza ushirikiano huo. Ameongeza kuwa kauli mbiu ya kanisa hilo “Kwa neema ya Mungu, tunajenga Huduma kwa vizazi vya sasa na vijavyo” inaakisi dhamira ya kuwekeza kwa kizazi cha sasa na kijacho.

Vile vile, Mhe. Sangu alisisitiza mambo matatu muhimu kwa Taasisi za dini ziendelee kuombea amani, mshikamano na afya njema kwa viongozi wakuu wa nchi akiwemo Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Kadhalika, amesema Serikali itaendelea kushirikiana na tasasisi za dini katika malezi ya vijana ili kujenga Taifa lenye maadili, upendo na uwajibikaji, pia kuendeleza ushirikiano katika utoaji wa elimu na huduma za kijamii kwa kizazi chenye uzalendo na uwajibikaji.

Aidha, Mhe. Sangu aliongoza harambee ya kuchangia ujenzi wa Kanisa, Ofisi na ununuzi wa gari, ambapo katika harambee hiyo Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amechangia Shilingi Milioni 15 na Waziri Sangu amechangia Shilingi Milioni 5.

Naye, Askofu Daniely Liyaseke aliwashukuru viongozi wa Serikali, viongozi wa dini na waumini kwa mshikamano na ushirikiano, akisisitiza kuwa “ukiona kobe yupo juu ya mti, ujue kuna aliyempandisha.”

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. James Millya pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro Mhe. Fakih Lulandala, walipongeza uongozi wa Askofu Liyaseke na kusisitiza kuwa uwepo wa Dayosisi hiyo ni nguzo ya mshikamano wa kijamii na maendeleo ya kiroho.

Na Janeth Raphael MichuziTv Bungeni - Dodoma

Mbunge wa Viti Maalumu, Khadija Shaban Taya, amesema kuwa anawaheshimu wanaume kwa nafasi yao katika jamii kama baba na kaka, lakini ameeleza kuwa sehemu kubwa ya changamoto za mmomonyoko wa maadili inatokana na baadhi ya wanaume kushindwa kutekeleza ipasavyo majukumu yao ya kifamilia, hali inayosababisha wanawake kubeba mzigo mkubwa wa uangalizi wa familia.

Akichangia hoja hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya wizara ya Maendeleo ya jamii Jinsia Wanawake na Makundi maalum Kwa mwaka wa fedha 2026/27 amesema kuwa pale wanaume wanaposhindwa kusimama katika majukumu yao ya malezi na uongozi wa familia, wanawake hujikuta wakilazimika kutoka na kujitafutia kipato ili kuhakikisha watoto wanapata mahitaji ya msingi.

Amefafanua kuwa hali hiyo imekuwa na athari za kijamii, ikiwemo kuongezeka kwa changamoto za malezi na kuporomoka kwa misingi ya maadili katika baadhi ya familia.

“Kwa hakika hakuna mwanamke mwenye akili timamu anayependa kumuumiza mwanaume anayempenda na kumheshimu. Wanawake wengi wanajikuta wakibeba majukumu makubwa kwa sababu ya mazingira yaliyopo,” amesema.

Aidha, Mbunge huyo ameeleza kuwa kuna baadhi ya wanaume wanaotelekeza familia zao, ikiwemo watoto wenye ulemavu, hali inayosababisha wanawake kuachwa peke yao katika mzigo wa malezi na matunzo.

Ameongeza kuwa katika baadhi ya familia, watoto wenye ulemavu wamekuwa wakikosa msaada wa baba zao, jambo linalosababisha changamoto kubwa kwa akina mama wanaojitahidi kuwalea na kuwahudumia bila msaada wa karibu wa kifamilia, wakati mwingine hata kukumbana na kutengwa na baadhi ya ndugu na jamii.

Katika wito wake kwa Serikali, Khadija Shaban Taya ameiomba kuangalia kwa karibu kundi la watoto wenye ulemavu na wazazi wao, ili kuhakikisha wanajumuishwa kikamilifu katika sera na mipango ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, ili kurahisisha upatikanaji wa huduma na utekelezaji wa haki zao.


Na Said Mwishehe,Michuzi TV


KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) Dk.Asha-Rose Migiro amejibu maswali mbalimbali aliyoulizwa na Mtangazaji Salim Kikeke kutoka Crown Media.

Kikeke amemuuliza maswali mbalimbali Dk.Migiro ambayo kwa sehemu kubwa yalijikita katika ripoti ya Tume ya kuchunguza vuruga kabla na baada ya Oktoba 29 ambayo iliongozwa na Mwenyekiti wake Jaji Mkuu mstaafu Othman Chande.

Nakuletea maswali matano kati ya maswali mengi aliyoulizwa

Dk.Migiro na kuyajibu kwa ufasaha na weledi mkubwa.Majibu ambayo yanathibitisha uwezo na umahiri wake katika uongozi hasa kwa kutambua historia yake ya uongozi kitaifa na kimataifa.Maswali hayo yalikuwa hivi;


Kikeke:Chama Cha Mapinduzi kimekuwa kimya kwa muda mrefu tangu ripoti ya Jaji chande kutoka, kwanini imekuwa kimya na kwanini sasa mmekubali kuzungumza na sisi?

Dk.Migiro: Ningependa kuliweka jambo hili katika muktadha sahihi , mtambuka vurugu za Oktoba 29 ni tukio ambalo lilitusitua wengi na sisi wana CCM tulishutuka zaidi kwani haijawahi kutokea katika taifa letu.

Tulipata mshangao, kulikuwa na kuduwaa na kulikuwa na kutafuta muda wa kulitafakari kwa kina nini kimetupata sisi Tanzania baada ya miaka mingi ya kuwa nchi yenye utulivu, amani na mshikamano

Kwahiyo ilichukua muda, na ilituhitaji kuitafakari hotuba ile ya Jaji Chande ambayo ilitokana na kazi waliyoifanya yeye na wana Tume wenzake.Kwahiyo ilichukua muda lakini baadae Chama kilizungumza kidogo kupitia Katibu wa Itikadi na Uenezi Kenani Kihongosi

Naye alisema wazi kwanza tunapongeza kuanzishwa kwa tume ile ilikuwa hatua muhimu katika kurejesha nchi yetu kwenye mstari.Pili alishukuru tume kwa kazi waliyofanya , kazi ambayo wameifanya kwa weledi mkubwa na mpaka sasa inaendelea kuwa sehemu ya namna ya sisi kubaini nini kilitokea na twendeje

Vilevile aliwashukuru wananchi , kwasababu kazi ya tume isingekamilika kama wananchi wasingejitokeza wakaunga mkono, wakatoa maoni yao.Kwahiyo ilikuwa hatua muhimu.

Lakini leo hii umetaka kuongea na sisi ni fursa nzuri na wakati muafaka na mimi Katibu Mkuu kueleza zaidi kuhusu muelekeo wetu kama Chama Cha Mapinduzi kuhusu taarifa ile twendeje kama Taifa na mengineyo ambayo utaona yanafaa

Kikeke:Umezungumza aliyosema Katibu Mwenezi,mnaunga mkono taarifa iliyotolewa na Tume ya Jaji Chande?


Dk.Migiro: Kwanza CCM tumepokea taarifa hii kwa umakini mkubwa na kwa kujua kwamba ni hatua muhimu sana tunataka kujua nini kilitokea kwasababu tunataka suala hili lisijirudie na Chama Cha Mapinduzi kingependa kufuatilia kwa karibu sana hatua gani zitafuata baada ya tume kutoa taarifa yake.Ni wakati muafaka kabisa kwa sisi CCM kuzungumza kupitia sauti ya Katibu Mkuu

Kikeke: Chama Cha Mapinduzi katika mkutano wake wa Halmashauri Kuu Taifa walionekana kuvipongeza vyombo vya ulinzi na usalama katika matukio ya Oktoba 29 , watu waliuawa katika siku ile ,kwanini mlifanya vile?


Dk.Migiro:Kwanza kabisa niseme tunaendelea kuonesha masikitiko yetu makubwa sana kwa vifo vilivyotokea .Vinapotokea vifo au hata kifo kimoja ni suala zito .Katika taarifa yake Mheshimiwa Jaji Chande alieleza kwamba tume ilibaini kuna watu takribani 518 waliopoteza maisha pamoja na madhara mengine yamejitokeza.

Kwahiyo Chama Cha Mapinduzi tunachukua hili suala kwa masikitiko makubwa sana na wako wengine wanaosema idadi hiyo ni ndogo labda ingekuwa kubwa lakini tutakumbuka tume ilitueleza na sisi Chama Cha Mapinduzi hatuna sababu ya kutia shaka vyanzo vyao ndio viliwapa taarifa ile.

Walisema walipata taarifa kupitia hospitali binafsi ,hospitali za serikali, Msajili wa Vizazi na vifo.Zote hizi zimeonesha watu 518 ndio waliopoteza maisha lakini walitutahadharisha inawezekana idadi ile ikabadilika kwasababu wako ambao hawakwenda hospitali wala hawakuandikisha.Sasa kwa Chama Cha Mapinduzi uhai wa mtu mmoja ni uhai mkubwa ambao hatuwezi kupima kwa namba

Kwa maana hiyo tumesikitika sana. Sasa kuhusu vyombo vya ulinzi na usalama ndugu Kikeke unafahamu katika nchi yeyote na Tanzania haina tofauti ,vyombo vya ulinzi na usalama vina kazi zake, vina jukumu ,tukizungumzia Polisi mojawapo ya majukumu yake makubwa ni kulinda usalama wa raia na mali zao.

Jeshi la Wananchi wa Tanzania linakazi kubwa ya kulinda mipaka ya nchi yetu,majukumu yake ya msingi ndio hayo sio kuua wananchi na tunafahamu tarehe 29 Oktoba nchi nzima tulikuwa na vituo vya kupigia kura takribani 99,000.

Na kwakuwa tuliamka katika hali ya kawaida wenzetu wanaolinda usalama wa raia walikuwa tayari wamekaa kwenye maeneo ya kupiga kura kwasababu wananchi waliowengi walikuwa wamejitayarisha kutoka kwenda kupiga kura na kurejea nyumbani.

Sasa ilipotokea kadhia ile vyombo hivi na hasa polisi walilazimika kujigawa huku usalama uendelee kuwepo kwenye maeneo ya kupiga kura na huku waje katika yale maeneo yaliyokuwa na fujo na pia itakumbukwa fujo hii ilikuwa kama moto wa nyikani , pale fujo huku fujo,sio Dar es Salaam peke yake ni katika nchi nzima kwa ujumla.

Kwahiyo hawa walikuwa kama wana jambo kubwa la kufanya kuhakikisha kura zinaendelea kupigwa na vile vile usalama katika maeneo mengine.Hilo lilikuwa jukumu lao kubwa na walilifanya na tunaamini kama wasingefanya vile labda madhara yangekuwa makubwa zaidi katika taifa letu.

Na pili ambalo naweza kuliunganisha hapo kwanini pia Chama Cha Mapinduzi kupitia halmashauri kuu tuliwapongeza. Kwasababu kazi waliyoifanya ndio imefanya taifa letu liwe imara mpaka leo pamoja na ile fujo ambayo kwanza hatukuitegemea lakini pia haijwahi kutokea.

Kwahiyo ilitushangaza wote tukapigwa na butwaa na kitu ambacho ningependa tutenganishe hapa inawezekana katika utendaji wa kazi zao kukawa na dosari hiyo inatokea, sasa tusichanganye majukumu yao ya msingi.Kazi nzuri waliyoifanya ya kutunza amani kwa kiwango kile ambacho kilihitajika kwa wakati ule na dosari moja moja zinazojitokeza…

Na hapa sisemi vifo ni dosari ndogo, sio dosari ndogo ni kubwa lakini ndio sababu kuna haja sasa ya kuangalia mazingira ya vifo vile lakini haindoi ukweli kazi waliyofanya ni ya kutukuka katika Taifa letu.


Kikeke:Mheshimiwa Katibu Mkuu inaonekana kama vile vyombo vya dola na hasa polisi vinaingia kwenye siasa kama kukilinda Chama Cha Mapinduzi ,kwanini?


Dk.Migiro:Hebu niambie siasa gani Jeshi la Polisi inafanya ikiashiria wanakilinda Chama Cha Mapinduzi?


Kikeke :Inaonekana kama inazuia wananchi wasitekeleze haki zao kwa kukitetea Chama.

Dk.Migiro:Si kweli ,kwanza kwa kuwa tunazungumzia masuala ya chaguzi ningependa kukumbusha katika mchakato wote wa uchaguzi katika Jamhuri ya Muungano, iwe Bara au Zanzibar hakukua na hali ambayo Jeshi la Polisi ililazimika kuingia kutuliza fujo au kudhibiti waliokuwepo.

Hii inaonesha vyama vyote vilifanya shughuli zao kwa utulivu kabisa na utakumbuka Mwenyekiti wetu wa Chama Cha Mapinduzi Dk.Samia Suluhu Hassan ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania siku ya uzinduzi wa kampeni alisema tunataka tufanye kampeni za kistaarabu,za tulivu ili kuwapa wananchi fursa ya kusikiliza Ilani ya vyama vyetu kusikiliza jinsi tunavyonadi sera zetu, na ahadi zetu na hatimaye siku ikifika wapige kura.

Kwa maana hiyo kulikuwa na utulivu nchi nzima, kwahiyo hapo sioni Chama Cha Mapinduzi kimelindwa vipi lakini kama nilivyosema mwanzo vyombo hivi ni vya taifa na vinawajibu kwa wananchi wake wote wakiwemo wanachama wa Chama Cha Mapinduzi na vyama vingine.


Kikeke:Taarifa ya Tume imesema watu waliuawa kwa kupigwa risasi Oktoba 29 , kwanini mpaka sasa hakuna viongozi wa Serikali ya CCM ambao wamewajibika?

Dk.Migiro:Awali ya yote ninawajibu wa kusema Chama Cha Mapinduzi na Watanzania walio wengi taarifa za kifo zimetusikitisha sana , Jaji Chande alipokuwa anazungumza ametoa takwimu kuna watu takribani 518 ambao waliuawa.

Namba ambayo inatusononesha na alisema inaweza kuongezeka na walitupa vyanzo vyao kwamba kulikuwa na taarifa za hospitali binafsi ,hospitali za Serikali , Msajili wa Vizazi na Vifo ndio zilitoa namba hizi na wamesema inawezekana namba hii ikabadilika kwasababu wako ambao hawakwenda hospitali wala hawakwenda kusajili vifo.

Kikeke: Lakini Mheshimiwa Balozi swali langu lilikuwa kwanini hakuna mtu ndani ya Serikali ya Chama Cha Mapinduzi ambaye amewajibika mpaka hivi sasa kwa yaliyotokea?

Dk.Migiro:Uwajibikaji ni suala muhimu sana na sisi Chama Cha Mapinduzi matumaini yetu yako kwenye tume ya uchunguzi wa jinai ambayo kazi yake itatoa mwanga zaidi katika suala la uwajibikaji ni muhimu .Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Dk.Samia Suluhu Hassan ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano alieleza wazi hakuna mtu aliyejuu ya sheria.

Kwa maana hiyo suala la uwajibikaji linanafasi kubwa sana ndani ya Chama Cha Mapinduzi na msisitizo huo tumeupata sio tu kwenye taarifa ya Tume na hata kwa kiongozi mkuu wa taifa letu .



Kama vipi tuwasiliane tupige stori
kuhusu majibu ya Dk.Migiro
0713833822





Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Benezeth Lutege, akizungumza wakati wa ufunguzi wa Warsha ya Uandaaji wa Rasimu ya Mkakati wa Kitaifa wa Mawasiliano Wakati wa Dharura kwa Huduma za Mifugo Tanzania, kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bi. Agness K. Meena. Warsha hiyo imefanyika leo Juni 1, 2026, katika Ukumbi wa Masailand Hall jijini Arusha.



Mkurugenzi Msaidizi wa Epidemiolojia na Magonjwa ya Mifugo Yanayovuka Mipaka (TADs) akitoa mchango wake katika majadiliano ya Warsha ya Uandaaji wa Rasimu ya Mkakati wa Kitaifa wa Mawasiliano Wakati wa Dharura kwa Huduma za Mifugo Tanzania, iliyofanyika leo Juni 1, 2026, jijini Arusha.



Afisa Habari II wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bi. Chiku Makwai, akitoa mchango wake katika majadiliano ya Warsha ya Uandaaji wa Rasimu ya Mkakati wa Kitaifa wa Mawasiliano Wakati wa Dharura kwa Huduma za Mifugo Tanzania, iliyofanyika leo Juni 1, 2026, jijini Arusha.



Afisa Sheria I wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bw. Denis Ukaka, akitoa mchango wake katika majadiliano ya Warsha ya Uandaaji wa Rasimu ya Mkakati wa Kitaifa wa Mawasiliano Wakati wa Dharura kwa Huduma za Mifugo Tanzania, iliyofanyika leo Juni 1, 2026, jijini Arusha.



Na Chiku Makwai – ARUSHA

Shirika la Afya ya Wanyama Duniani (WOAH), kwa kushirikiana na Wizara ya Mifugo na Uvuvi, limeanza mchakato wa kuandaa Rasimu ya Mkakati wa Kitaifa wa Mawasiliano Wakati wa Dharura kwa Huduma za Mifugo Tanzania, hatua inayolenga kuimarisha uwezo wa nchi katika kuzuia, kudhibiti na kukabiliana na milipuko ya magonjwa ya mifugo.

Warsha ya kuandaa rasimu hiyo imefunguliwa leo, Juni 1, 2026, katika Ukumbi wa Masailand Hall jijini Arusha na Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo, Dkt. Benezeth Lutege, kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Agness K. Meena.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa warsha hiyo, Dkt. Lutege amesema mawasiliano yenye ufanisi ni nyenzo muhimu katika kudhibiti na kukabili milipuko ya magonjwa ya mifugo kwa kuwa huwezesha utoaji wa taarifa sahihi kwa wakati kwa wadau wote wanaohusika.

Amesema Serikali inaendelea kuimarisha mifumo ya tahadhari na mwitikio wa haraka ili kuhakikisha magonjwa ya mifugo yanagunduliwa na kudhibitiwa mapema kabla hayajasababisha athari kubwa kwa uzalishaji, biashara ya mifugo na afya ya jamii.

“Mkakati huu utaweka msingi wa kuwa na mfumo mmoja wa kitaifa wa mawasiliano ya dharura utakaoongoza utoaji wa taarifa, ushirikishwaji wa wadau na usimamizi wa mawasiliano wakati wa matukio ya milipuko ya magonjwa ya mifugo,” amesema Dkt. Lutege.

Aidha, amebainisha kuwa magonjwa mbalimbali ya mifugo, ikiwemo Homa ya Bonde la Ufa (Rift Valley Fever), yanahitaji uratibu madhubuti wa mawasiliano ili kuhakikisha wananchi na wadau wanapata taarifa sahihi zitakazowawezesha kuchukua hatua stahiki kwa wakati.

Warsha hiyo imewakutanisha wataalamu wa mifugo, afya ya wanyama, mawasiliano na wadau wengine kutoka taasisi za Serikali pamoja na mashirika ya kimataifa kwa lengo la kujadili mbinu bora za mawasiliano ya hatari, usimamizi wa taarifa za dharura na mikakati ya kuimarisha mwitikio wakati wa milipuko ya magonjwa.

Washiriki pia wanatarajiwa kujadili matumizi ya teknolojia za kisasa katika utoaji wa taarifa pamoja na namna ya kuimarisha ushirikiano kati ya sekta ya afya ya wanyama na afya ya binadamu kwa kuzingatia dhana ya Afya Moja (One Health).

Kupitia warsha hiyo, Tanzania inatarajia kuwa na mkakati madhubuti wa mawasiliano ya dharura utakaosaidia kuimarisha mifumo ya tahadhari ya mapema, kuongeza mwitikio wa haraka wakati wa matukio ya dharura na kulinda ustawi wa mifugo sambamba na kuchangia maendeleo ya uchumi wa taifa.



MBUNGE wa Kisarawe, Dkt. Selemani Jafo,akichangia hotuba ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum leo Juni 1,2026 bungeni jijini Dodoma.



MBUNGE wa Kisarawe, Dkt. Selemani Jafo,akichangia hotuba ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum leo Juni 1,2026 bungeni jijini Dodoma.

......

MBUNGE wa Kisarawe, Dkt. Selemani Jafo, ameitaka Serikali kuboresha mazingira ya kazi kwa Maafisa Maendeleo ya Jamii nchini ikiwemo kuwapatia magari ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi.

Akichangia hotuba ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum bungeni, Dkt. Jafo amesema maafisa hao ni nguzo muhimu katika kusukuma maendeleo ya jamii na wanastahili kuwezeshwa kwa vitendea kazi vinavyokidhi mahitaji ya kazi zao.

Amesema Maafisa Maendeleo ya Jamii ni mawakala wa mabadiliko katika jamii kwa kuwa karibu kila programu ya maendeleo inayotekelezwa nchini inahitaji ushiriki wao wa moja kwa moja, hivyo ni muhimu kupewa heshima na mazingira bora ya kufanyia kazi.

Dkt. Jafo ameeleza kuwa pamoja na magari, maafisa hao wanapaswa kuwa na ofisi zenye hadhi na rasilimali za kutosha zitakazowawezesha kuwafikia wananchi kwa urahisi na kutoa huduma stahiki.

Aidha, ameishauri Serikali kuanzisha vitengo vya Maendeleo ya Jamii katika wizara zote na taasisi za umma zaidi ya 325 ili kuhakikisha masuala ya maendeleo ya jamii yanapewa kipaumbele na kuratibiwa kwa ufanisi katika sekta mbalimbali.

Pia amependekeza kuanzishwa kwa Kitengo cha Uratibu wa Sekta ndani ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii kitakachosaidia kuunganisha taarifa za maendeleo kutoka wizara na taasisi mbalimbali, hatua ambayo alisema itaiwezesha nchi kuwa na mfumo imara wa kufuatilia maendeleo ya wananchi na taifa kwa ujumla.

Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma 

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima, amesema Serikali imeweka mkazo mkubwa katika malezi, makuzi na ustawi wa watoto kama msingi wa kujenga Taifa lenye maadili, mshikamano na maendeleo endelevu kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Akiwasilisha bungeni hotuba ya mapitio ya utekelezaji wa Mpango na Bajeti ya mwaka 2025/26 pamoja na makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka 2026/27, Dkt. Gwajima alisema Wizara yake imejipanga kutekeleza vipaumbele saba vya kimkakati vitakavyochochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa manufaa ya Watanzania wote.

Ameeleza kuwa katika mwaka wa fedha 2026/27, Wizara itajikita katika maeneo yenye uwezo mkubwa wa kuleta mageuzi ya kijamii na kiuchumi, huku ikilenga kujenga Tanzania yenye jamii imara, jumuishi na inayozingatia maendeleo endelevu.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, kipaumbele cha kwanza kitakuwa ni kujenga mtaji watu wa Taifa na kuandaa kizazi cha Tanzania ya mwaka 2050 kitakachozingatia maadili, uzalendo, haki, usawa, ustawi na maendeleo jumuishi. Alisema Serikali inaamini kuwa watu ndiyo rasilimali muhimu zaidi katika safari ya maendeleo ya Taifa.

Aidha, amebainisha kuwa Serikali itaendelea kuimarisha huduma za ustawi, malezi na makuzi ya watoto pamoja na mifumo ya ulinzi wa kijamii ili kuhakikisha kunakuwa na Taifa lenye mshikamano, uthabiti na utu wa kibinadamu.

Katika eneo la usawa wa kijinsia, Dkt. Gwajima amesema Serikali itaendelea kuimarisha mifumo ya uwezeshaji wa wanawake na kupambana na vitendo vya ukatili wa kijinsia ili kuhakikisha wanawake wanashiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo na uchumi wa Taifa.

Pia ameeleza kuwa Wizara inalenga kufanya mageuzi ya kiuchumi kwa makundi maalum na sekta isiyo rasmi kwa kuwasaidia wananchi kutoka katika uchumi wa kujikimu na kuingia katika uchumi rasmi wa kibiashara wenye tija, ushindani na mchango mkubwa katika pato la Taifa.

Kwa upande wa matumizi ya teknolojia, Waziri huyo alisema Serikali itaongeza matumizi ya mifumo ya kidijitali na takwimu katika utoaji wa huduma za kijamii ili kurahisisha utendaji kazi na kuhakikisha maamuzi yanafanyika kwa kuzingatia ushahidi wa kitakwimu.

Ameongeza kuwa juhudi pia zitaelekezwa katika kujenga jamii yenye amani, uwajibikaji na mshikamano pamoja na kuimarisha ushirikiano wa kimkakati kati ya Serikali, Asasi za Kiraia, sekta binafsi, taasisi za dini na wadau wa maendeleo.

Dkt. Gwajima amesema kupitia vipaumbele hivyo, Serikali inalenga kujenga jamii salama na yenye ustawi, wanawake wenye nguvu kiuchumi, watoto waliopata malezi bora, pamoja na uchumi jumuishi unaochochewa na maarifa, teknolojia na ubunifu.

Amesisitiza kuwa bajeti ya Wizara hiyo imeweka kipaumbele katika huduma za ustawi wa jamii, uratibu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, huduma kwa watoto, wazee, wanawake, wanaume na makundi mengine maalum, akibainisha kuwa huduma hizo ni sehemu muhimu ya kulinda amani, usalama na uthabiti wa Taifa.

“Hatutapima mafanikio ya bajeti hii kwa kiasi cha fedha kilichotumika pekee, bali kwa matokeo yatakayopatikana kwa familia, wananchi na Taifa kwa ujumla,” alisema.

Katika sehemu ya hotuba yake iliyovuta hisia za wabunge, Waziri huyo aliweka msisitizo mkubwa kwenye suala la malezi ya watoto, akisema ndilo jambo linalobeba mustakabali wa Tanzania kuliko jambo jingine lolote.

Ameeleza kuwa pamoja na uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali katika miundombinu mbalimbali ikiwemo reli za kisasa, bandari, viwanja vya ndege na miji ya kisasa, mafanikio hayo hayatakuwa na maana ikiwa Taifa litashindwa kujenga watoto wenye maadili, nidhamu, uzalendo, utu na uwezo wa kushindana katika dunia ya mwaka 2050.

“Taifa lolote hujengwa kwanza kwenye malezi kabla halijajengwa kwenye uchumi. Mtoto wa leo ndiye mtendaji wa Serikali wa kesho, daktari wa kesho, mwalimu wa kesho, jaji wa kesho, askari wa kesho, mwekezaji wa kesho na kiongozi wa Taifa wa kesho,” alisema.

Ameonya kuwa kuharibu malezi ya watoto wa leo ni sawa na kuharibu Tanzania ya kesho, akisisitiza umuhimu wa familia, jamii na taasisi mbalimbali kushiriki kikamilifu katika kuhakikisha watoto wanalelewa katika misingi ya maadili mema, uzalendo na uwajibikaji.

Dkt. Gwajima alihitimisha kwa kueleza kuwa utekelezaji wa mpango na bajeti ya mwaka 2026/27 umeandaliwa mahsusi kuleta matokeo yanayopimika, kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma, kupunguza umaskini, kulinda makundi yaliyo hatarini na kuimarisha mshikamano wa Kitaifa kuelekea kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.






-Yalenga Kuimarisha Ufanisi wa Chama

Na Oscar Assenga,TANGA

Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Tanga kimeongeza kasi ya utekelezaji wa mradi wake wa ujenzi wa nyumba 36 za watumishi baada ya Mwenyekiti wa chama hicho mkoani humo, Rajab Abdulrahman, kukabidhi shilingi milioni 500 kwa ajili ya kukamilisha mradi huo unaotekelezwa katika wilaya tisa za mkoa huo.

Fedha hizo zilikabidhiwa kwa Katibu wa CCM Mkoa wa Tanga, Mfaume Kizigo, katika hatua inayodhihirisha dhamira ya chama ya kuboresha mazingira ya kazi na makazi kwa viongozi wake wa ngazi za wilaya.

Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Rajab alisema mradi huo unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Desemba mwaka huu na kwamba utakuwa na mchango mkubwa katika kuimarisha utendaji wa watumishi pamoja na shughuli za chama katika maeneo mbalimbali ya mkoa.

Alieleza kuwa mradi huo una thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 2.5, huku fedha zote zinazohitajika kwa ajili ya utekelezaji wake zikiwa tayari zimepatikana kupitia michango ya wanachama, viongozi na wadau mbalimbali wa chama.

"Mradi huu unagharimu jumla ya shilingi bilioni 2, milioni 500 na laki 250. Fedha hizi zimepatikana kupitia michango mbalimbali ikiwemo milioni 56 zilizotolewa awali, milioni 10 kutoka kwa MNEC pamoja na michango iliyokusanywa kutoka wilaya zote za mkoa," alisema Rajab.

Mwenyekiti huyo alibainisha kuwa kukamilika kwa nyumba hizo kutasaidia kutatua changamoto za makazi kwa baadhi ya viongozi wa chama katika ngazi ya wilaya, jambo litakaloongeza utulivu wa kazi, uwajibikaji na ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Alisema nyumba hizo si tu kwamba zitakuwa makazi ya viongozi, bali pia ni uwekezaji wa muda mrefu wa chama katika kujenga taasisi imara yenye uwezo wa kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kuendelea kuwahudumia wanachama wake.

"Tunajenga misingi ya chama kwa vizazi vya sasa na vijavyo. Viongozi wanaweza kubadilika, lakini miundombinu tunayojenga leo itaendelea kulitumikia chama kwa miaka mingi ijayo," alisisitiza.

Rajab aliongeza kuwa ujenzi wa chama ni jukumu endelevu linalohitaji mshikamano wa wanachama wote, akisisitiza kuwa maendeleo ya chama hayawezi kupatikana bila ushiriki wa pamoja wa wanachama wake.

Kutokana na hilo, aliwataka wana-CCM wa Mkoa wa Tanga kuendelea kuchangia kwa hali na mali, kutumia elimu na uzoefu wao pamoja na nguvu kazi katika kukiimarisha chama.

Kwa upande wake, Katibu wa CCM Mkoa wa Tanga, Mfaume Kizigo, alisema mradi huo ni sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa chama wa kuimarisha utendaji wake katika ngazi za wilaya kwa kuhakikisha viongozi wanapata mazingira bora ya kazi na makazi.

Alifafanua kuwa kila wilaya imepangiwa kujenga nyumba nne ambazo zitatumika na viongozi muhimu wa chama na jumuiya zake.

"Kila wilaya imepangiwa kujenga nyumba nne ambazo ni nyumba ya Katibu wa CCM wa Wilaya, nyumba ya Katibu wa Jumuiya ya Vijana, nyumba ya Katibu wa Jumuiya ya Wazazi pamoja na nyumba ya Katibu wa UWT," alisema Kizigo.

Alieleza kuwa uwepo wa nyumba hizo utasaidia kupunguza gharama za upangaji wa makazi, kuimarisha upatikanaji wa viongozi katika maeneo yao ya kazi na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa shughuli za chama na jumuiya zake.

Kwa mujibu wa Kizigo, kukamilika kwa mradi huo kutakuwa hatua muhimu katika kuijengea CCM Mkoa wa Tanga miundombinu imara itakayosaidia kuendeleza shughuli zake za kisiasa, kiutawala na kijamii kwa ufanisi zaidi katika miaka ijayo.

Mradi wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) ya Unenepeshaji wa Mbuzi na Kilimo cha Malisho, ambao unatekelezwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo, umepanga kuwawezesha wanawake na vijana 6000 ndani ya muda wake wa utekelezaji wa Miaka Mitano wa Mradi huo, ambao ukiwa na lengo la kuongeza ushiriki wa wanawake na vijana katika ujasiliamali wa Biashara ya Mifugo.

Akizungumza leo Juni 1, 2026 Mkoani Morogoro, katika Warsha ya Upitiaji, Uhakiki wa Uwasilishaji wa Ripoti ya awali ya Jinsia na Ujumuishaji wa Kijamii katika Programu hiyo ya BBT, Meneja Mradi wa BBT Upande wa Jinsia na Ujumuishaji wa Kijamii, Bi. Neema Urassa amesema Mradi huo una lengo la kuwawezesha Wanawake na Vijana kupitia shughuli za unenepeshaji wa Mbuzi na Kondoo kibiashara pamoja na Kilimo cha Malisho ya Mifugo.

"Mradi huu unawalenga zaidi Wanawake na vijana, ambao kupitia Mradi huu watapata kujifunza vitu mbalimbali kwa vitendo katika mnyororo mzima wa thamani wa mazao ya mifugo, hususan mbuzi na Kondoo na Kilimo cha Malisho ya Mifugo, ili baadae wawe na uwezo wa kuingia kwenye biashara za unenepeshaji wa mifugo kwa lengo la kujiongezea kipato pamoja na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa." Amesema Bi. Urassa

Aidha, Bi. Urassa amesema baada ya vijana kupata ujuzi huo, matarajio ya Serikali ni kuwa vijana wataweza kujiajiri wenyewe, kuanzisha biashara zao, na kuwa sehemu ya suluhisho la changamoto ya ajira nchini, ambapo vijana watakaonufaika watakuwa na fursa ya kupatiwa mikopo isiyo na dhamana kwa ajili ya kuendeleza biashara zao baada ya mafunzo.

Vilevile, Bi. Urassa,  ameweka wazi kuwa Mradi huo unatokana na Uongozi madhubuti wa Serikali ya Awamu ya Sita wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kutambua kwa kina changamoto ya ukosefu wa ajira miongoni mwa vijana, ndiyo maana Mheshimiwa Rais amechukua juhudi za makusudi kuhakikisha fedha hizo zinapatikana kwa ajili ya kuboresha maisha ya vijana kupitia miradi yenye tija kama huo wa BBT ambao unaendana na Dira ya Taifa ya Mwaka 2050.







Farida Mangube, Morogoro

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) imezindua jengo jipya la Ofisi ya Mkoa wa Morogoro lililogharimu Shilingi bilioni 1.63, huku ikitoa wito kwa wananchi kuongeza ushiriki katika usimamizi wa miradi ya maendeleo ili kuhakikisha thamani ya fedha za umma inaonekana na mianya ya rushwa inazibwa.

Akizindua jengo hilo Juni 1, 2026, Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Bw. Crispin Francis Chalamila, amesema uwekezaji unaofanywa na Serikali katika ujenzi wa ofisi za taasisi hiyo unaonesha dhamira ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Sita katika kuimarisha mapambano dhidi ya rushwa nchini.

Amesema Serikali imeendelea kuiwezesha TAKUKURU kwa rasilimali watu, vitendea kazi na fedha za kujenga miundombinu ya kisasa, hatua inayolenga kuboresha mazingira ya kazi kwa watumishi na utoaji wa huduma kwa wananchi.

“Kwa idadi ya majengo yanayojengwa na yaliyokwishajengwa, ni wazi kuwa Serikali imefanya uwekezaji mkubwa katika kuimarisha taasisi hii. Huu ni ushahidi wa dhamira yake ya kuendelea kupambana na rushwa nchini,” amesema Chalamila.

Amebainisha kuwa TAKUKURU ina jumla ya ofisi 145 nchini, zikiwemo ofisi za mikoa 28, wilaya 111 na vituo maalumu sita. Hata hivyo, kati ya hizo, ni ofisi 70 pekee zinazomilikiwa na taasisi hiyo, huku ofisi 64 zikiendelea kutumia majengo yasiyomilikiwa na TAKUKURU.

Kwa mujibu wa Mkuu wa huyo wa TAKUKURU, katika mwaka wa fedha 2025/2026 taasisi hiyo inaendelea kujenga majengo 11 mapya, likiwemo jengo moja la mkoa na majengo 10 ya wilaya.

“Morogoro ni miongoni mwa mikoa iliyobahatika kufikiwa mapema katika mpango huu wa ujenzi wa majengo ya kudumu ya TAKUKURU,” aMEsema.

Awali, akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa mradi huo, Mkurugenzi wa Kitengo cha Usimamizi wa Milki wa TAKUKURU, Dkt. Emmanuel Kiyabo, amesema mradi huo ulitekelezwa kwa gharama ya Shilingi 1,627,857,615.81, ikiwa ni ongezeko la Shilingi milioni 27.8 kutoka bajeti ya awali ya Shilingi bilioni 1.6.

Ameeleza kuwa ongezeko hilo la asilimia 1.74 lilitokana na maboresho ya kiufundi yaliyofanyika wakati wa utekelezaji wa mradi, ikiwemo kuongeza mota za kufungua na kufunga mageti yote mawili ya uzio, kuongeza eneo la paving blocks na kazi za kuboresha eneo la kuingilia kutoka barabarani.

Dkt. Kiyabo amesema mradi ulianza Machi 6, 2025 na ulitarajiwa kukamilika Januari 5, 2026, lakini ulikamilika Machi 30, 2026 baada ya kuchelewa kwa takribani miezi mitatu.

Alitaja sababu za kuchelewa kwa mradi kuwa ni uhaba wa mabati ya kuezekea, kuchelewa kupatikana kwa vifaa vya ukuta wa vioo, mvua za masika pamoja na kusitishwa kwa baadhi ya shughuli kufuatia mazingira yaliyojitokeza wakati wa uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.

Mradi huo ulitekelezwa kwa mfumo wa Design and Build kupitia ushirikiano kati ya TAKUKURU na Shirika la Magereza (PCS), ambapo wataalamu kutoka taasisi hizo walihusika katika usanifu, usimamizi na utekelezaji wa kazi za ujenzi.

Jengo hilo limejengwa katika eneo la Kihonda Kilimanjaro Manispaa ya Morogoro na linajumuisha jengo kuu la ofisi lenye ghorofa moja, nyumba ya walinzi, nyumba ya jenereta na miundombinu mingine ikiwemo tenki la maji la lita 60,000, mnara wa matenki ya maji, uzio wa kisasa na eneo la maegesho na bustani.

Katika hotuba yake, Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU amewataka watumishi wa TAKUKURU kuyatunza majengo mapya yanayojengwa na Serikali ili yaweze kudumu na kuendelea kutoa huduma kwa muda mrefu.

Aidha, alitoa wito kwa wananchi kushirikiana na TAKUKURU katika kusimamia matumizi ya fedha za umma zinazotengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo.

Alisema halmashauri zinapaswa kuhakikisha wananchi wanapata taarifa za miradi inayotekelezwa pamoja na fedha zinazotumika ili kuongeza uwazi na uwajibikaji.

“Ni muhimu wananchi wakafahamu miradi inayotekelezwa katika maeneo yao na kushiriki kuifuatilia. Hii itasaidia kuhakikisha thamani ya fedha inaonekana na kuzuia mianya ya rushwa,” alisema.

Pia alisisitiza umuhimu wa kuendelea kutoa elimu dhidi ya rushwa kwa vijana kupitia Klabu za Wapinga Rushwa shuleni, akieleza kuwa kujenga kizazi kinachochukia rushwa ni msingi muhimu wa mafanikio ya mapambano hayo kwa siku zijazo.

Uzinduzi wa jengo hilo ulihudhuriwa na viongozi wa Mkoa wa Morogoro, Kamati ya Usalama ya Mkoa, watumishi wa TAKUKURU, wanafunzi wa Klabu za Wapinga Rushwa pamoja na wadau mbalimbali wa maendeleo.







RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametoa usafiri wa ndege kwa ajili ya kuwachukua mashujaa wa Timu ya Taifa ya Vijana chini ya umri wa Miaka 17 (Serengeti Boys), baada ya kufuzu kucheza  fainali ya Michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Vijana (AFCON U-17, 2026).

 Ndege hiyo itaondoka  leo,  Juni Mosi,  2026,  saa 5:00 usiku, kuelekea nchini Morocco, na itarejea Jumatano tarehe 03 Juni 2026. 

Msafara huo utaongozwa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda  akiwa ameambatana na viongozi wa Serikali pamoja na Timu ya Taifa ya Mpira wa Miguu (Taifa Stars), lengo ikiwa ni kuongeza nguvu, morali na hamasa kwa Serengeti Boys katika hatua hiyo muhimu. 

Waziri Makonda amemshukuru  Rais Samia kwa kuendelea kuwekeza katika maendeleo ya michezo nchini pamoja na uamuzi huo wa kurahisisha safari ambayo itaongeza hamasa kwa vijana na kuimarisha uzalendo. Pia amewasisitiza Watanzania 

kuendelea kuiunga mkono, kuishangilia na kuiombea heri Serengeti Boys katika fainali dhidi ya Senegal. 

Mchezo huo wa fainali utachewa Juni 02 2026 nchini Morocco, saa 4:00 usiku kwa saa za Afrika Mashariki, ukiwa ni  mchezo wa kihistoria kwa Tanzania na unatarajiwa kuvuta hisia za mashabiki wengi barani Afrika.

Aidha, Taifa Stars itatumia fursa hiyo kushiriki michezo ya kirafiki ya kimataifa dhidi ya timu zitakazokuwa kwenye kalenda ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Duniani  (FIFA), kama sehemu ya maandalizi ya mashindano yajayo.



Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete, amesema Serikali itaendelea kusimamia kwa nguvu zote maadili, uwajibikaji na uadilifu katika Utumishi wa Umma ili kuhakikisha huduma zinazotolewa kwa wananchi zinakuwa bora, zenye tija na zinazoendana na matarajio ya maendeleo ya taifa.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha Wakuu wa Vitengo na Idara za Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu kutoka taasisi mbalimbali za Serikali, Ridhiwani amesema Utumishi wa Umma una mchango mkubwa katika kufanikisha agenda ya maendeleo ya Taifa, hivyo ni muhimu watumishi wote kuzingatia misingi ya uadilifu, uzalendo na uwajibikaji katika kutekeleza majukumu yao.

Aidha amesisitiza kuwa suala la maadili Serikali imeanza kuchukua hatua kali dhidi ya watumishi wanaojihusisha na vitendo vya kughushi nyaraka za kiutumishi pamoja na ukiukwaji mwingine wa maadili ya kazi.

Amebainisha kuwa tayari watuhumiwa sita wamefikishwa mahakamani na wanakabiliwa na mashtaka yanayohusiana na uhujumu uchumi kutokana na vitendo vyao vya kughushi nyaraka za kiutumishi.

“Tunataka Utumishi wa Umma wenye uadilifu, uwajibikaji na uzalendo. Hakuna nafasi ya rushwa, kughushi nyaraka au kutumia vibaya madaraka ya umma. Serikali itaendelea kuchukua hatua stahiki kwa yeyote atakayebainika kwenda kinyume na maadili ya utumishi,” alisema Ridhiwani.

Amesema matumizi ya teknolojia na mifumo ya kisasa katika usimamizi wa rasilimaliwatu ni nyenzo muhimu katika kuongeza uwazi, kuimarisha utendaji kazi na kudhibiti mianya ya ukiukwaji wa maadili ndani ya taasisi za umma.

Waziri huyo amewataka wataalamu wa rasilimaliwatu nchini kuendelea kuwa nguzo muhimu katika mageuzi ya Utumishi wa Umma kwa kuhakikisha sheria, kanuni na taratibu za kiutumishi zinasimamiwa kwa haki na usawa.

Amesisitiza kuwa wataalamu hao wanapaswa kuwa mstari wa mbele katika kuijenga Tanzania ya mwaka 2050 kwa kuimarisha mifumo ya utawala bora, kuhamasisha uwajibikaji na kuhakikisha watumishi wanatekeleza majukumu yao kwa ufanisi unaolenga matokeo.

“Tunapoelekea Tanzania ya mwaka 2050, tunahitaji Utumishi wa Umma unaosimamia haki, uwazi, usawa na matumizi sahihi ya teknolojia. Hili linawezekana endapo wataalamu wa rasilimaliwatu watasimamia kikamilifu misingi ya utawala bora katika maeneo yao ya kazi,” alieleza.

Kikao kazi hicho kimewakutanisha Wakuu wa Vitengo na Idara za Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu kutoka taasisi mbalimbali za Serikali kwa lengo la kujadili namna ya kuimarisha usimamizi wa rasilimaliwatu, kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi na kuimarisha uwajibikaji katika Utumishi wa Umma.

Kaulimbiu ya kikao hicho ni “Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu katika Utumishi wa Umma Sikivu, Jumuishi, Wenye Matokeo na Uwajibikaji kuelekea Tanzania ya 2050.”






Wananchi wa Kijiji cha Mkungugu jimbo la Ismani katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa mkoani Iringa wakiwa katika foleni ya kupiga kura ya kumchagua Mbunge wao katuika uchaguzi mdogo uliyofanyika leo Juni 01, 2026.

Mwananchi Mkazi wa wa Kijiji cha Kihongorota katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa mkoani Iringa, Angelista Mwenda akipiga kura katika uchaguzi mdogo wa Ubunge jimbo la Ismani uliofanyika leo Juni 01, 2026.
Mwananchi Mkazi wa wa Kijiji cha Kihongorota katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa mkoani Iringa, Angelista Mwenda akipiga kura katika uchaguzi mdogo wa Ubunge jimbo la Ismani uliofanyika leo Juni 01, 2026.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele akipita kuingia katika kituo cha Kura cha Ofisi ya Kijiji Mtera katika jimbo la Ismani Wilaya ya Iringa mkoani Iringa kukagua mwenendo wa zoezi la kupiga kura kwa wananchi wa Ismani lililofanyika leo Juni 01, 2026.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele akizungumza na Mawakala katika moja ya vituo alivyotembelea.
MWENYEKITI wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi Jaji wa Mahakama ya Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele amesema zoezi la upigaji Kura wa Ubunge katika jimbo la Isman katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa Mkoani Iringa na Kata 12 za Tanzania Bara limekwenda vizuri.

Mwenyekiti huyo wa Tume Jaji Mwambegele amesema hayo leo Juni 01,2026 akiwa katika ofisi za Kijiji Igingilanyi Wilayani Iringa mara baada ya kutembelea na kukagua zoezi la upigaji Kura linavyoendelea katika vituo vya kupigia Kura vya jimbo la Isimani ambako kunafanyika uchaguzi mdogo wa ubunge.

Amesema mwitikio wa wananchi wa Ismani katika kujitokeza kupiga kura umekua mkubwa na hata katika Kata nyingine 12 ambazo nazo zinachagua Madiwani hii leo wamejitokeza kwa Wingi.

Mwenyekiti huyo wa Tume Jaji Mwambegele ameshudia upigaji kura kwa baadhi yavituo vilivyopo katika vijiji vya Igingilanyi, Mkungugu, Kihongorota na Migori.

Kata 12 zilofanya uchaguzi leo ni Mzimuni iliyopo Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni; Zongomera, Halmashauri ya Manispaa ya Kahama; Itilo, Halmashauri ya Mji Nzega; Ketare, Halmashauri ya Mji Tarime na Nyumbigwa, Halmashauri ya Mji Kasulu.

Nyingine ni Kata ya Kala iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi; Ziba, Halmashauri ya Wilaya Igunga; Kamsisi, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele; Nyamugali, Halmashauri ya Wilaya ya Buhigwe; Namasakata Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru; Bwongera, Halmashauri ya Wilaya ya Chato na Kibiti, Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti.


Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele akikagua mwenendo wa zoezi la kupiga kura kwa wananchi wa Jimbo la Ismani lililopo Halmashauri ya Iringa mkoani Iringa hii leo Juni 01,2026.



Wananchi wakiwa katika mistari tayari kuingia vituoni kupiga Kura.




Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele akikagua mwenendo wa zoezi la kupiga kura kwa wananchi wa Jimbo la Ismani lililopo Halmashauri ya Iringa mkoani Iringa hii leo Juni 01,2026.



Wananchi wakiwa katika mistari tayari kuingia vituoni kupiga Kura.


Top News