Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, amekutana na ujumbe wa kampuni ya madini ya AngloGold Ashanti kujadili maendeleo ya shughuli za kampuni hiyo na namna ya kuimarisha uhusiano wake na Tanzania.

Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, alifanya mazungumzo hayo Jumanne, Septemba 1, 2026, wakati ujumbe wa AngloGold Ashanti ulipomtembelea ofisini kwake jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kumweleza maendeleo ya shughuli za kampuni hiyo na maslahi yake ya kibiashara nchini Tanzania.

Ujumbe huo uliongozwa na Bi. Lizelle Marwick, Afisa Mkuu wa Sheria wa AngloGold Ashanti, na ulijumuisha Balozi Baso Sangqu, Makamu wa Rais Mwandamizi anayeshughulikia Uendelevu wa AngloGold Ashanti, pamoja na Bw. Simon Shayo, Makamu wa Rais anayeshughulikia Uendelevu na Ushirikishwaji wa wadau wa Geita Gold Mining Limited (GGML).

AngloGold Ashanti ni mojawapo ya kampuni kubwa duniani katika sekta ya madini na inafanya shughuli zake nchini kupitia kampuni tanzu ya GGML.

Akizungumza na ujumbe huo, Bw. Mchechu alisema OTR, kama mwakilishi wa Serikali katika umiliki wa hisa, ni mshirika mwenza wa kampuni hiyo, akisisitiza kuwa mafanikio ya biashara yana manufaa kwa pande zote mbili.

“Nyie msipopata matokeo, na sisi hatupati matokeo; na nyie mkipata matokeo, na sisi tunapata matokeo,” alisema.

Alisema OTR inafanya kazi kwa karibu na mamlaka husika, huku taasisi hizo zikiwa na mtazamo mmoja kuhusu masuala muhimu ili kutengeneza mazingira rafiki zaidi ya uwekezaji.

Bw. Mchechu alisema OTR inalenga kujenga uhusiano wa muda mrefu na AngloGold Ashanti unaozingatia uelewano, utawala bora wa kampuni na mafanikio endelevu ya biashara.

Alisisitiza pia umuhimu wa kuwa na bodi za wakurugenzi zenye watu wenye uwezo, uelewa wa biashara na mtazamo wa kimkakati, akibainisha kuwa wajumbe wa bodi wanapaswa kuwa na uwezo wa kuongeza thamani katika uendeshaji na mwelekeo wa kampuni, hususan katika taasisi zinazochangia kodi na gawio kwa Serikali.

Kwa upande wake, Bi. Marwick alisema AngloGold Ashanti inathamini uhusiano wake na Serikali za nchi ambako inafanya shughuli zake, huku akieleza kuwa kampuni hiyo inatambua umuhimu wa uhusiano wake wa muda mrefu na Serikali ya Tanzania.

Alisema kampuni hiyo inalenga kujenga ushirikiano wa kweli unaowezesha kila upande kutumia uwezo na uzoefu wake katika kutengeneza matokeo yenye manufaa kwa kampuni na nchi kwa ujumla.

Katika kuimarisha uelewa na uwezo wa wajumbe wa bodi, Bi. Marwick alisema AngloGold Ashanti iko tayari kushirikiana katika programu za mafunzo na utangulizi wa majukumu ya bodi, zitakazohusu wajibu wa wajumbe, taratibu za uendeshaji wa bodi na uelewa wa masuala ya fedha.

Pia alipendekeza wajumbe wa bodi kufanya ziara katika Mgodi wa Dhahabu wa Geita ili kupata uelewa wa moja kwa moja kuhusu shughuli za uchimbaji, pamoja na masuala ya kitaalamu yanayohusu rasilimali na akiba ya madini.

Alisema uhusiano mzuri uliopo kati ya kampuni hiyo na Serikali unaweza kuwa msingi muhimu wa kuendeleza shughuli zake katika maeneo mengine yenye leseni za utafiti nchini, kwa kuwa kampuni inaweza kupanua shughuli zake kwa urahisi zaidi katika mazingira ambayo tayari ina shughuli, miundombinu na uhusiano mzuri wa kikazi na Serikali.





Na Janeth Raphael -MichuziTv -Bungeni Dodoma 


SERIKALI imeeleza mikakati mbalimbali inayotekelezwa katika kuendeleza michezo kwa watu wenye ulemavu, ikiwemo kuandaa makocha, kuendesha mashindano na matamasha ya michezo, pamoja na kuwawezesha wanamichezo wenye ulemavu kushiriki mashindano ya kimataifa.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Nyamizi Simon Mhoja, aliyetaka kujua mkakati wa Serikali wa kuendeleza michezo kwa watu wenye ulemavu na kuzalisha wachezaji wenye ulemavu.

Waziri Makonda amesema Serikali kupitia Baraza la Michezo la Taifa (BMT) imeendelea kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata fursa ya kushiriki na kuendeleza vipaji vyao katika michezo.

Amesema hatua hizo ni pamoja na kuandaa makocha wa michezo kwa watu wenye ulemavu, kuendesha matamasha yanayowashirikisha, kuandaa mashindano ya ndani ya michezo mbalimbali, pamoja na kuwezesha wanamichezo wenye ulemavu kushiriki mashindano ya kimataifa.

Aidha, Waziri Makonda amesema Serikali imeendelea kuhamasisha uanzishaji na usajili wa vyama vya michezo kwa watu wenye ulemavu, hatua inayolenga kuimarisha usimamizi na maendeleo ya michezo hiyo nchini.

Hadi Agosti 2026, jumla ya vyama tisa (9) vya michezo kwa watu wenye ulemavu vimesajiliwa, vikihusisha michezo mbalimbali ikiwemo soka, mpira wa kikapu, tenisi, riadha na kuogelea.

Hatua hizo zinaelezwa kuwa sehemu ya jitihada za Serikali za kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata mazingira bora ya kugundua, kukuza na kutumia vipaji vyao katika michezo, ndani na nje ya Tanzania.


Na Janeth Raphael - MichuziTv- Bungeni Dodoma

SERIKALI imesema kima cha chini cha mshahara katika sekta binafsi nchini huwekwa kwa kuzingatia sekta za kiuchumi pamoja na vigezo mbalimbali vya kisheria, huku ikisisitiza kuwa utaratibu huo haujajengwa kwa lengo la kubagua wafanyakazi wa kampuni za kigeni na zile za kizawa.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano) Deus Sangu wakati akijibu swali la Mbunge wa Kuteuliwa, Mheshimiwa Abdulliah Ali Mwinyi, aliyehoji iwapo Serikali haioni kuwa utofauti wa viwango vya kima cha chini cha mshahara kati ya kampuni za kigeni na za kizawa unaweza kutengeneza tabaka katika jamii.

Katika swali lake, Mbunge huyo alitaka kujua kama Serikali haioni kuwa kanuni zinazoweka viwango tofauti vya mishahara kwa kampuni za kigeni na za kizawa zinaweza kuleta ubaguzi katika ajira na malipo ya wafanyakazi.

Akijibu, Waziri amesema kima cha chini cha mshahara kinawekwa kwa mujibu wa Sheria ya Taasisi za Kazi, Sura ya 300, ambayo imeanzisha Bodi za Kima cha Chini cha Mshahara kwa kuzingatia sekta mbalimbali za uchumi.

Waziri Sangu amesema katika Sekta Binafsi, Bodi ya Kima cha Chini cha Mshahara ina jukumu la kufanya tafiti kuhusu hali ya ajira na uchumi na kumshauri Waziri mwenye dhamana ya masuala ya kazi kuhusu kiwango kinachopaswa kuwekwa na kutangazwa kwa sekta husika.

Waziri amesema kima cha chini cha mshahara katika sekta binafsi nchini hakipangwi kwa mtazamo wa kampuni kuwa ya kigeni au ya kizawa pekee, bali huzingatia sekta za kiuchumi ambazo waajiri na wafanyakazi wanafanyia kazi.

Aidha, amesema katika kupanga viwango hivyo, Serikali huzingatia vigezo mbalimbali vilivyowekwa na mikataba ya kimataifa pamoja na sheria za nchi, ikiwemo uwezo wa waajiri kufanya biashara na kulipa ujira unaostahili.

Kigezo kingine kinachozingatiwa, kwa mujibu wa Serikali, ni gharama za maisha, jambo linalolenga kuhakikisha viwango vya mishahara vinazingatia mazingira halisi ya kiuchumi yanayowakabili wafanyakazi na waajiri.

Kauli hiyo ya Serikali imekuja wakati ambapo suala la tofauti za mishahara katika sekta binafsi likiwa miongoni mwa hoja zinazogusa usawa katika ajira, uwezo wa waajiri na ustawi wa wafanyakazi.

Serikali imeendelea kusisitiza kuwa upangaji wa kima cha chini cha mshahara unapaswa kuzingatia hali ya uchumi, gharama za maisha na uwezo wa waajiri, huku ukiendana na matakwa ya sheria za nchi na mikataba ya kimataifa ya kazi.



-Ni katika Wiki ya Ubunifu Tanzania (IWTz) 2026

Katika Wiki ya Ubunifu Tanzania (IWTz) 2026, Vodacom Tanzania imeonyesha mchango wa mtandao, ubunifu na ujasiriamali katika kufanikisha Dira ya Maendeleo Tanzania 2050. Tukio hilo limewakutanisha wabunifu, wajasiriamali, watunga sera, wawekezaji, vijana na wadau mbalimbali chini ya kauli mbiu: “Kutoka Matarajio hadi Mageuzi: Kuibua Njia ya Tanzania Kuelekea Ustawi Jumuishi.”

Vodacom imeshiriki katika mjadala kuhusu uchumi wa watengeneza maudhui, maonesho, mikutano na wadau na shughuli za kuelimisha kuhusu usalama wa mtandao.

Akizungumza katika mjadala wa watengeneza maudhui na majukwaa mtandaoni, Mkuu wa Idara ya Chapa na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania, Yvonne Maruma, alisema mtandao una thamani zaidi kupitia fursa unazowawezesha Watanzania kuzipata katika elimu, biashara na ubunifu.

Kupitia Vodacom Youth Base (VYB), kampuni inaendelea kuwawezesha watengeneza maudhui kubaki mtandaoni na kukuza shughuli zao za kidijitali. Ushiriki wa Vodacom katika IWTz 2026 unaunga mkono malengo ya Dira ya Maendeleo 2050 kupitia mageuzi ya kidijitali, uvumbuzi na ukuaji wa uchumi jumuishi.
Mkuu wa Idara ya Chapa na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania Yvonne Maruma akizungumza katika Wiki ya Ubunifu Tanzania 2026 ambapo alizungumzia namna ya Vodacom inavyounganisha Watanzania na kuleta tija kupitia Zaidi ya Mtandao: Hususani Watengeneza maudhui na Majukwaa Mtandaoni kwa kuwapa mtandao bora na simu janja zinazo unga mkono ubunifu wao.

Mkuu wa Idara ya Chapa na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania Yvonn Maruma (kulia) akisalimiana na Naibu Katibu Mkuu wa Tume ya Taifa ya Mipango Dr. Blandina Kilama baada ya kumaliza majadiliano ya namna ya kuziunganisha sauti za Watanzania: Watengeneza maudhui na Majukwaa Mtandaoni. Tukio hilo limefanyika katika Wiki ya Ubunifu Tanzania leo hii.

Mkuu wa Idara ya Chapa na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania Yvonne Maruma (kulia) akisalimiana na Mhariri Mtendaji mkuu wa kampuni ya Mwananchi Communications Limited baada ya kumaliza majadiliano ya namna ya kuziunganisha sauti za Watanzania: Watengeneza maudhui na Majukwaa Mtandaoni. Tukio hilo lilifanyika katika Wiki ya Ubunifu Tanzania leo hii.

Mkuu wa Idara ya Chapa na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania Yvonne Maruma (wa pili kushoto), akisikiliza majadiliano yaliyohusu namna ya kuziunganisha sauti za Watanzania: Watengeneza maudhui na Majukwaa Mtandaoni. Tukio hilo lilifanyika wakatib wa Wiki ya Ubunifu Tanzania.

Mkuu wa Idara ya Chapa na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania Yvonne Maruma (kulia), Mkurugenzi Mtendaji wa Mwananchi Communications Limited Rosalynn Mndolwa-Mworia (wa pili wa kushoto), Meneja wa Uchunguzi wa Vodacom Tanzania Joseph Mnyune (kushoto) na Meneja Biashara Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Mwananchi Communication Limited Tess Aloyce (wa pili kulia) wakizungumza wakati wa Wiki ya Ubunifu Tanzania ambapo Vodacom Tanzania walishiriki katika majadiliano ya namna ya kuziunganisha sauti za Watanzania: Watengeneza maudhui na Majukwaa Mtandaoni. Tukio hilo lilifanyika katika Wiki ya Ubunifu Tanzania leo hii.


 

 

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imetangaza kushuka kwa bei za bidhaa za mafuta kwa mwezi Septemba 2026. Bei ya petroli imeshuka kwa Shilingi 102 kwa lita, huku bei ya dizeli ikishuka kwa Shilingi 101 kwa lita. Bei hizo zitaanza kutumika kuanzia tarehe 2 Septemba 2026, saa 6:01 usiku.

EWURA inaendelea kufuatilia kwa karibu mwenendo wa bei za mafuta katika soko la dunia, ambapo mabadiliko ya bei yanaendelea kuathiriwa pamoja na mambo mengine na hali ya kiusalama katika eneo la Mashariki ya Kati.

Kwa mujibu wa Sheria ya Mafuta ya Mwaka 2015, bei za mafuta zinaendelea kupangwa kwa kuzingatia mfumo wa soko. Wafanyabiashara wote wa rejareja wanatakiwa kuuza mafuta kwa bei zisizozidi bei elekezi, na wananchi wanashauriwa kutoa taarifa EWURA kwa kituo chochote cha mafuta kitakachouza zaidi ya bei elekezi.


‎JUKWAA Huru la Wahariri Tanzania (JUWATA) na Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC) wamekubaliana kuimarisha ushirikiano katika kulinda uhuru wa vyombo vya habari, kutetea haki na maslahi ya waandishi wa habari pamoja na kuhakikisha jamii inapata habari sahihi na kwa wakati.

‎‎Makubaliano hayo yamefikiwa katika kikao cha pamoja cha viongozi wa JUWATA na UTPC kilichofanyika katika ofisi za UTPC zilizopo Barabara ya Aboud Jumbe, Mtaa wa Kazembo, eneo la Uzunguni jijini Dodoma.

‎Katika kikao hicho, viongozi hao walijadili masuala mbalimbali yanayohusu sekta ya habari, ikiwemo umuhimu wa kuwa na mshikamano miongoni mwa wadau wa habari katika kukabiliana na changamoto zinazowakabili waandishi wa habari na vyombo vya habari nchini.

‎Aidha, walisisitiza umuhimu wa taasisi hizo kushirikiana katika kutetea uhuru wa vyombo vya habari, haki za waandishi wa habari na maslahi yao, huku wakitambua nafasi muhimu ya wanahabari katika kuhabarisha, kuelimisha na kuwajibika katika jamii.

‎Ushirikiano huo pia unalenga kuongeza nguvu katika kushughulikia changamoto zinazohusu mazingira ya kazi ya waandishi wa habari, pamoja na kujenga mahusiano mazuri kati ya wadau wa habari na taasisi mbalimbali zinazohusika na maendeleo ya sekta hiyo.

‎UTPC ina jumla ya Klabu 28 za Waandishi wa Habari zinazowakilisha waandishi wa habari kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, hivyo kuwa na mtandao mpana wa kuwafikia wanahabari katika maeneo mbalimbali nchini.

‎Kwa upande wa JUWATA, ujumbe uliongozwa na Mwenyekiti wake, Richard Mwaikenda, akifuatana na Makamu Mwenyekiti, Sylivester Ngombaniza, pamoja.

‎UTPC iliwakilishwa na Mkurugenzi Mtendaji, Kenneth Simbaya, pamoja na Afisa wa Programu wa Ufuatiliaji Rasilimali, Andrew Malawiti, Kaimu Afisa wa Fedha Winfrida Madeni na Afisa Msaidizi wa Programu, Edmund Kapungu.

‎Viongozi hao wameeleza umuhimu wa kuendeleza mawasiliano na ushirikiano wa karibu baina ya taasisi hizo kwa manufaa ya waandishi wa habari, vyombo vya habari na jamii kwa ujumla.

‎Wamesisitiza kuwa mshikamano wa wadau wa habari ni muhimu katika kujenga sekta imara, yenye weledi na inayoweza kutekeleza kwa ufanisi wajibu wake wa kuhabarisha umma na kulinda maslahi mapana ya jamii.


‎ ...........,...............


‎Jukwaa Huru la Wahariri Tanzania (JUWATA) limeanzishwa kihalali kwa kuzingatia Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, likiwa na lengo la kupanua wigo kwa Wahariri wanaotimiza vigezo kuwa huru kujiunga na jukwaa hilo, ili kuongeza nguvu, umoja na ushirikiano katika kutetea na kulinda haki na maslahi ya Waandishi wa Habari pamoja na jamii kwa ujumla.

‎Katika kutekeleza majukumu yake ya kila siku, JUWATA itazingatia Katiba na kanuni zake, sambamba na kufuata na kuheshimu Sheria za Nchi pamoja na taratibu zinazotawala tasnia ya Habari.

‎Kwa ufupi, JUWATA haijaasisiwa kwa lengo la kupambana, kushindana au kusigana na taasisi nyingine za Habari.

‎Badala yake, inalenga kujenga ushirikiano, mshikamano na mahusiano mema na taasisi za Habari za ndani na nje ya nchi, kwa manufaa ya Wahariri, Waandishi wa Habari na jamii kwa ujumla.

‎JUWATA inaamini kuwa umoja, ushirikiano na kuheshimiana ndiyo msingi wa kujenga tasnia imara, huru, yenye uwajibikaji na inayoweza kusimamia kwa ufanisi haki na maslahi ya Wadau wa Habari.
Mkurugenzi Mtendaji wa Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC, Kenneth Simbaya (katikati) akiwa na Mwenyekiti wa Jukwaa Huru la Wahariri Tanzania (JUWATA. Richard Mwaikenda pamoja na Makamu Mwenyekiti wa jukwa hilo, Sylivester Ngombaniza baada ya kufanya kikao hicho.
Kutoka kushoto ni Makamu Mwenyekiti wa JUWATA,Ngombaniza,Kaimu Afisa wa Fedha, Winfrida Madeni, Mwenyekiti wa JUWATA, Mwaikenda, Mkurugenzi Mtendaji wa UTPC, Simbaya na Afisa wa Programu UfuatiliajiRasilimali, Andrew Malawiti.
Viongozi wa JUWATA na UTPC wakiwa katika kikao hicho.

Mwaikenda akimsikiliza kwa makini Simbaya wakati wa kikao hicho.

Mwaikenda akizungumza wakati wa kikao hicho.
Simbaya akiagana na viongozi wa JUWATA.

Mbio za Mwenge wa Uhuru 2026 leo Sep 1,26 Umeangazia  mafanikio makubwa ya Sekta Binafsi Wilaya ya Bukoba Vijijini kupitia uwekezaji wa Kiwanda cha kuchakata Parachichi cha "BallyVado"

Hii ni katika kutambuai mchango mkubwa wa sekta binafsi katika kukuza sekta ya kilimo-biashara (agribusiness) mkoani humo, ambapo kilimo cha parachichi kimekuwa kikikua kwa kasi kubwa..

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Ndg.Wazo M. Mwang'onda, ametoa pongezi za dhati kwa Mkurugenzi wa Kiwanda hicho Mzee Depson Balyagati kwa kuwa na maono ya mbali na kuthubutu kuwekeza mamilioni ya fedha katika miundombinu ya kisasa ya kuchakata matunda hayo.

Aidha Ndugu Mwang'onda amebainisha kuwa nchi inahitaji wawekezaji wazawa wenye uzalendo kama wa Mkurugenzi Mzee Depson  Balyagati, ambao hawaangalii faida yao tu, bali wanaangalia jinsi ya kuwasaidia wakulima wadogo vijijini kupata soko la uhakika.Kwa upande wake,

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kitanda hicho Mzee Dspson Balyagati( Mnec Mstaafu) amesema kuwa uamuzi wa kujenga kiwanda hicho ulitokana na kuguswa na changamoto ya wakulima wa Bukoba kuona mazao yao yakipotea kwa kukosa masoko baada ya kuvuna. Na kusisitiza kuwa kiwanda chake sasa kipo tayari kununua parachichi zote za kiwango cha soko la kimataifa.

Naye Mbunge wa Bukoba Vijijini, Dkt. Jasson Rweikiza, ambaye alimpongeza Mkurugenzi Balyagati kwa kuleta kiwanda hicho karibu na wananchi, akiahidi kuwa uongozi wa jimbo utaendelea kuhamasisha kilimo cha parachichi ili kiwanda kisikose malighafi wakati wote wa uzalishaji.

#BallyVadoOil #MwengeWaUhuru2026 

#BokobaToTheWorld









Na Mwandishi wa OTR

Dar es Salaam. Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, amekutana na kufanya mazungumzo na wawakilishi wa Barrick Corporation, mwanahisa mwenza wa Twiga Minerals Corporation Limited (TWIGA), pamoja na uongozi wa TWIGA, kujadili maendeleo na masuala mbalimbali yanayohusu uendeshaji wa miradi inayosimamiwa na kampuni hiyo.

Mazungumzo hayo yalifanyika Jumanne, Septemba 1, 2026, wakati ujumbe wa Barrick ulipofanya ziara katika Ofisi ya Msajili wa Hazina (OTR), jijini Dar es Salaam.

Ujumbe wa Barrick uliongozwa na Roelie Gey Von Pittius, Meneja wa Fedha wa Barrick kwa Afrika na Mashariki ya Kati, akiambatana na Candace Simpson, Meneja wa Kodi wa Afrika na Mashariki ya Kati; Melkiory Ngido, Meneja wa Barrick nchini Tanzania; na Judith Chambua, Meneja wa Kodi wa Barrick Tanzania.

Katika kikao hicho, Serikali, kupitia OTR, na Barrick, ambao ni wanahisa wenza wa TWIGA, walijadili masuala mbalimbali yanayohusu maendeleo na uendeshaji wa miradi ya uchimbaji wa dhahabu inayomilikiwa kwa ubia kupitia TWIGA.

Miongoni mwa miradi iliyojadiliwa ni pamoja na migodi ya North Mara na Bulyanhulu, pamoja na Buzwagi, ambao kwa sasa upo katika hatua za mwisho za kufungwa.

Uongozi wa TWIGA pamoja na wataalamu kutoka Barrick walishiriki katika kikao hicho kwa kutoa taarifa na ufafanuzi kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu maendeleo na uendeshaji wa miradi hiyo.

Akizungumza katika kikao hicho, Bw. Mchechu alisema Serikali, kupitia Ofisi ya Msajili wa Hazina, itaendelea kutoa ushirikiano unaohitajika katika kutatua changamoto mbalimbali zinazoweza kujitokeza katika uendeshaji wa miradi ya TWIGA, kwa lengo la kuhakikisha miradi hiyo inaendelea kwa ufanisi, kuongeza uzalishaji na kuchangia zaidi katika uchumi wa Taifa.

Aidha, Bw. Mchechu alisisitiza kuwa sekta ya madini inaendelea kuwa na mchango mkubwa katika uchumi wa Taifa na mapato ya Serikali, ikiwemo kupitia gawio linalotokana na uwekezaji wa Serikali katika kampuni za madini.

Bw. Mchechu alisema Serikali inathamini ushirikiano wake na Barrick na inaendelea kutumia uzoefu uliopatikana kupitia uhusiano huo katika kuimarisha sekta ya madini nchini.

“Tunauthamini sana mchango wa aina ya ushirikiano tulionao na Barrick,” alisema.

Alisema Barrick imekuwa mshirika muhimu katika maendeleo ya sekta ya madini nchini na kwamba ushirikiano huo umeiwezesha Serikali kupata uzoefu katika kusimamia uwekezaji mkubwa katika sekta hiyo.

Bw. Mchechu alisema Serikali inaendelea kufanya mashauriano na taasisi zinazohusika ili kuhakikisha masuala yanayohusu uwekezaji na shughuli za kampuni hiyo yanashughulikiwa kwa ufanisi na kwa uelewa wa pamoja.

“Katika masuala muhimu kama haya yanayomhusu mshirika muhimu katika biashara muhimu, ni lazima serikali izungumze kwa sauti moja,” alisema.

Alisema Serikali inalenga kujenga mazingira yatakayowezesha uwekezaji kuendelea kukua na kutoa manufaa ya muda mrefu kwa Tanzania.

“Tunataka kuwa na biashara ambayo inaweza kuendelea kwa utulivu kizazi hadi kizazi na kustahimili tawala mbalimbali za kisiasa,” alisema.

Kwa upande wake, Von Pittius alisema Barrick inaendelea kuthamini ushirikiano wake na Serikali na inaendelea kushirikiana na mamlaka husika katika masuala yanayohusu shughuli zake nchini.

Bw. Von Pittius alieleza nia ya kuendelea kushirikiana katika masuala mbalimbali yenye maslahi kwa uwekezaji na maendeleo ya sekta ya madini nchini.

Mazungumzo ya Jumanne ni sehemu ya mwendelezo wa ushirikiano kati ya Serikali na Barrick katika kuimarisha mazingira ya uwekezaji na shughuli za madini nchini.








Na Said Mwishehe,Michuzi TV




MAMLAKA ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya(DCEA)imezindua Klabu za kupiga vita dawa za kulevya katika vyuo vikuu nchini ikiwani sehemu ya juhudi za Serikali za kuimarisha ushiriki wa jamii hususani wanafunzi wa vyuo vikuu katika kudhibiti na kupambana na tatizo la dawa za kulevya

Hatua ambayo pia inalenga kuimarisha kinga, kuongeza uelewa na kujenga mazingira yatakayosaidia vijana kufanya maamuzi salama na yenye tija kwa mustakabali wa maisha yao na Taifa kwa ujumla.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa klabu hizo leo Septemba 1,2026 katika ukumbi wa Maktaba Mpya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ,Kamishna Jenerali wa Mamlaka hiyo Aretas Lyimo amesema vilabu hivyo vitatumika pia kutafakari kwa mtizamo wa kitaaluma kuhusu tatizo la dawa za kulevya.

Pia athari zake kwa vijana wa kizazi kipya kwani uraibu ni tatizo linalopoteza utu na kusababisha mateso kwa vijana. “Katika kubabiliana na tatizo hili, kunahitaji majibu ya kina na hatua za uzuiaji zinazohusisha jamii kikamilifu. Vilabu hivi vitatumika pia kwa kutoa elimu na kuhamasisha jamii kuhusu madhara ya dawa za kulevya.

“Tatizo la dawa za kulevya lina athari katika afya ya jamii, usalama, uchumi, familia na maendeleo ya Taifa. Kwa msingi huo, Serikali imeweka mikakati inayolenga kudhibiti biashara na matumizi ya dawa za kulevya.”

Amefafanua mikakati hiyo ni kupunguza upatikanaji wa dawa za kulevya, uhitaji wa dawa za kulevya, madhara yatokanayo na matumizi ya dawa za kulevya pamoja na kuimarisha ushirikiano wa kitaifa, kikanda na kimataifa.

“Tukio lililotukutanisha leo ni sehemu ya utekelezaji wa mkakati wa pili wa kupunguza uhitaji wa dawa za kulevya. Mkakati huu unasisitiza kinga kupitia elimu, uhamasishaji na hatua zinazolenga kuzuia watu kuanza kutumia dawa za kulevya.

“Katika utekelezaji wa mkakati huu, Mamlaka imeandaa muongozo wa utoaji elimu ambao umeainisha makundi yanayohitaji elimu kuhusu tatizo la dawa za kulevya. Wanafunzi wa Vyuo Vikuu ni miongoni mwa makundi hayo muhimu.

“Mamlaka imewalenga wanafunzi wa vyuo vikuu kwa sababu mko katika mazingira ambayo yanahitaji uelewa sahihi na uwezo wa kufanya maamuzi kuhusu masuala yanayoweza kuathiri afya, masomo na mustakabali wenu.

“Tumeshuhudia baadhi ya wanafunzi wa vyuo vikuu wakishindwa kuendelea na masomo yao kutokana na makundi rika na kutumbukia kwenye starehe na matumizi ya dawa za kulevya,”amesema Kamishna Jenerali Lyimo.

Ameongeza pia vyuo vikuu ni vituo vya kuzalisha wataalamu na maarifa yanayosaidia kutatua changamoto mbalimbali za kijamii. Kwa hiyo, elimu kuhusu dawa za kulevya inayotolewa kwa kundi hilo inalenga zaidi kuzuia matumizi ya dawa za kulevya miongoni mwa wanafunzi.

Amesisitiza lengo ni kujenga kizazi cha wataalamu kitakachoweza kulielewa tatizo hili kwa mtazamo wa kitaaluma na kulisaidia Taifa kupata suluhisho lenye ushahidi wa kisayansi ambalo linatumia akili mnemba (AI) na teknolojia katika kupunguza tatizo la dawa za kulevya nchini. Suluhisho la ubunifu wa kimkakati lenye tija kwa Taifa.

“Baada ya kupata elimu hii, Mamlaka inatarajia kuona wanafunzi na wataalamu wa vyuo vikuu wakishiriki katika tafiti kuhusu sababu na vihatarishi vya matumizi ya dawa za kulevya, mwenendo wa tatizo, madhara yake na ufanisi wa hatua zinazochukuliwa katika kukabiliana nalo.

“Tafiti hizo zitasaidia kuongeza uelewa wa Taifa kuhusu tatizo hili na kutoa msingi wa kuboresha sera, mipango na afua za Serikali. Lipo ombwe la tafiti za kisayansi na kitaaluma juu ya tatizo la dawa za kulevya kwa ujumla,”

Amesema hivyo anawahamasisha wanataaluma kujikita kwenye tafiti ili kupata majibu ya kisayansi na kitaaluma juu ya tatizo la dawa za kulevya.”Ninyi kama wataalamu wa afya, mtasaidia katika tafiti kuhusu madhara ya kiafya na tiba…

“Watalaam wa saikolojia na jamii wanaweza kuchunguza sababu zinazochochea matumizi, wataalamu wa sheria wanaweza kusaidia katika kuchambua changamoto za utekelezaji wa sheria huku wataalamu wa TEHAMA wakichangia matumizi ya teknolojia katika kupunguza uingiaji, uzalishaji na usambazaji wa dawa za kulevya”

Awali Mwakilishi wa Jumuiya ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (Vyuo vya kati na Vyuo Vikuu) Tanzania (TAHILISO) Aron Seni amesema vyuo hivyo ni vituo muhimu vya kuzalisha wataalamu na viongozi wa kesho.

Amefafanua lakini mazingira ya sasa yanaweza kuwaweka vijana katika hatari ya kushawishika kutumia dawa za kulevya kutokana na uhuru wa maisha ya chuoni, shinikizo kutoka kwa marafiki na changamoto za maisha.

“Tumeshuhudia baadhi ya vijana kutoka taasisi za elimu ya juu wakikamatwa, kufunguliwa mashtaka na wengine kuhukumiwa kwa makosa yanayohusiana na dawa za kulevya,” amesema.

Ameongeza baadhi ya wanafunzi huanza kutumia dawa hizo kwa majaribio, kushawishiwa na marafiki au kutokana na changamoto mbalimbali za maisha, hivyo hatua za mapema za kinga na elimu zinahitajika.

Amesisitiza klabu hizo hazipaswi kuwa vikundi vya kufanya shughuli za kawaida au kupiga picha kwa ajili ya mitandao ya kijamii, bali ziwe nguzo za elimu, ulinzi na ukombozi wa vijana.

“Klabu hizi zitatoa nafasi salama kwa wanafunzi wanaokabiliwa na changamoto za matumizi ya dawa za kulevya kupata elimu, ushauri na msaada bila kuhukumiwa.Tunaishukuru DCEA kwa ushirikiano uliowezesha kufanikisha mchakato huu.”














Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo,akizungumza wakati akiongoza kikao cha tafakuri cha uongozi na watumishi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kilicholenga kutathmini utekelezaji wa majukumu yaliyokabidhiwa kwa wizara.

Na.Mwandishi Wetu

Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo, amewapongeza watumishi wa wizara hiyo kwa kazi kubwa na mafanikio waliyoyapata katika mwaka wa fedha uliopita, huku akiwataka kuendelea kuyasema kwa ujasiri mafanikio hayo yaliyoiwezesha sekta ya elimu kung’aa kitaifa na kimataifa.

Prof. Nombo amesema mafanikio hayo yametokana na uongozi imara wa Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, na Naibu Waziri, Mhe. Wanu Hafidh Ameir, pamoja na ushirikiano wa Wakurugenzi, Wakuu wa Idara na watumishi wote.

Prof. Nombo amesema hayo Septemba 1, 2026 jijini Dodoma wakati alipoongoza kikao cha tafakuri cha uongozi na watumishi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kilicholenga kutathmini utekelezaji wa majukumu yaliyokabidhiwa kwa wizara. Amewashukuru watumishi kwa utekelezaji mzuri wa majukumu yao na kusisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano katika kufikia malengo ya wizara.

Aidha, Prof. Nombo amesema mabadiliko makubwa yanayoendelea katika sekta ya elimu yanatokana na utekelezaji wa sera mpya ya elimu, ambayo inalenga kuandaa wahitimu wenye ujuzi, kuboresha matokeo ya kujifunza na kuimarisha mfumo mzima wa elimu nchini. Amesisitiza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, imewekeza kwa kiwango kikubwa katika sekta ya elimu kupitia ujenzi wa miundombinu, ajira za walimu, mafunzo ya watumishi na fursa mbalimbali za kitaaluma.

Katika kikao hicho, Katibu Mkuu amekumbusha wajibu mkubwa wa Wizara katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, akieleza kuwa takribani asilimia 40 ya masuala yaliyomo kwenye dira hiyo yanahusu sekta ya elimu, sayansi, teknolojia na ubunifu. Ameongeza kuwa utekelezaji wa elimu ya lazima kwa miaka 10 na maandalizi ya kupokea kundi la wanafunzi la double cohort mwaka 2028 ni miongoni mwa majukumu makubwa yanayohitaji maandalizi ya mapema na ushirikiano wa pamoja.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Daniel Mushi, amewataka watumishi kuendelea kufanya kazi kwa ushirikiano, weledi, nidhamu na uadilifu, akisema misingi hiyo ni muhimu katika kuimarisha utendaji kazini. Prof. Mushi amesema hayo Septemba 1, 2026 jijini Dodoma wakati akifunga kikao cha tafakuri cha watumishi wa wizara hiyo.

Amesema mafanikio ya wizara yanatokana na mchango wa kila mtumishi, hivyo kuna umuhimu wa kuongeza ubunifu katika utendaji huku sheria, kanuni, taratibu na miongozo ya utumishi wa umma ikizingatiwa. Pia amesisitiza umuhimu wa kuzingatia usalama wa taarifa za Serikali na kuhakikisha wananchi wanahudumiwa kwa furaha, ufanisi na weledi, huku akiwataka watumishi kutumia mafunzo waliyopata kuongeza tija na kuhamasisha utamaduni wa kuendelea kujifunza katika kila ngazi ya utumishi.

Naye, Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Rasilimali Watu katika Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Edith Rwiza, amesema kikao cha uongozi na watumishi kimetoa fursa ya kutafakari kwa pamoja, kujenga mshikamano na kubadilishana uzoefu kwa lengo la kuimarisha utendaji kazi.

Amesema kikao hicho pia kililenga kutafakari mafanikio, changamoto na mafunzo yaliyopatikana katika utekelezaji wa mipango na majukumu ya wizara katika mwaka uliopita.

Dkt. Rwiza amesema kikao hicho kimewapa watumishi nafasi ya kujitathmini kwa kuzingatia uhalisia wa utendaji kazi na kujadili namna bora ya kuhakikisha malengo ya wizara yanafikiwa kwa ufanisi.

Ameongeza kuwa washiriki wamepata fursa ya kutazama kwa pamoja changamoto za rasilimali na kubaini namna ya kuongeza ufanisi ili kupata matokeov makubwa zaidi kwa kutumia rasilimali zilizopo, huku wakielekezwa kuimarisha mshikamano na uwajibikaji katika kutekeleza majukumu yao.



Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo,akizungumza wakati akiongoza kikao cha tafakuri cha uongozi na watumishi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kilicholenga kutathmini utekelezaji wa majukumu yaliyokabidhiwa kwa wizara.



Sehemu ya Watumishi wakimsikiliza Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo (hayupo pichani) wakati akiongoza kikao cha tafakuri cha uongozi na watumishi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kilicholenga kutathmini utekelezaji wa majukumu yaliyokabidhiwa kwa wizara.



Sehemu ya Watumishi wakimsikiliza Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo (hayupo pichani) wakati akiongoza kikao cha tafakuri cha uongozi na watumishi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kilicholenga kutathmini utekelezaji wa majukumu yaliyokabidhiwa kwa wizara.



Sehemu ya Watumishi wakimsikiliza Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo (hayupo pichani) wakati akiongoza kikao cha tafakuri cha uongozi na watumishi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kilicholenga kutathmini utekelezaji wa majukumu yaliyokabidhiwa kwa wizara.



Sehemu ya Watumishi wakimsikiliza Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo (hayupo pichani) wakati akiongoza kikao cha tafakuri cha uongozi na watumishi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kilicholenga kutathmini utekelezaji wa majukumu yaliyokabidhiwa kwa wizara.

Top News