Na. Mwandishi wetu, Sumbawanga
WADAU wa maendeleo ndani na nje ya mkoa wa Rukwa wamehamasishwa kuchangia upatikanaji wa madawati kwa ajili ya kuwezesha watoto kusoma kwenye mazingira wezeshi kwa ustawi wa taaluma.

Wito huo umetolewa hivi karibuni na Mbunge wa Jimbo la Kwela ambaye pia ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu wakati alipokabidhi madawati kwa shule za msingi katika jimbo hilo alipofanya ziara ya kikazi.

Katika ziara hiyo sangu alikabidhi madawati zaidi ya 100 kwa shule za msingi sita (6) yenye thamani ya shilingi Milioni 60 ambayo ameyapata kupitia ufadhili ya Benki ya Taifa ya Biashara (NBC).

Waziri Sangu akizungumza kwenye moja ya mikutano yake na wananchi wa kijiji cha Nankanga tarafa ya Kipeta na kijiji cha Ilemba alisema ametoa msaada huo kuunga mkono jitihanda za wananchi katika kuchangia maendeleo ya elimu.

“ Nimekuja hapa kukabidhi zawadi ndogo kwa Watoto.Leo nimewaletea madawati 20 ambapo yatasaidia Watoto 60 kutoendelea kukaa chini” alisema Waziri Sangu.

Mbunge huyo aliongeza kuwaambia wananchi kuwa yeye ni mbunge wa vitendo na kwamba anapenda vitu vinavyoonekana ambapo aliitumia fursa hiyo kushukuru uongozi wa Benki ya NBC kwa kuguswa na shida za wanaKwela .

“Ninashukuru benki ya NBC kwa msaada wao waliotupatia madawati haya yanayokwenda kupunguza tatizo la watoto kukaa chini. utatuzi huu wa kero za wananchi ni sehemu ya maelekezo tuliyopewa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwetu wabunge” alisema Sangu alipoongea na wananchi wa Kijiji cha Msia kata ya Milepa huku akitoa wito kwa wadau wengine wa maendeleo kuchangia madawati kwa ajili ya jimbo la Kwela.

Miongoni mwa shule zilizopokea madawati hayo na idadi yake kwenye mabano ni shule ya msingi Kalumbaleza (20), Msia (20), Kimambo (15), Ilemba (20) , Nankanga (20) na Deusi Sangu sekondari madawati (30).

Akizungumza kwa niaba ya wananchi, Diwani wa kata ya Mwadui Mahmood Leonce Mgweno alisema amepokea madawati toka Ofisi ya Mbunge na kwa tayari amefikisha shuleni na kumpongeza Mbunge Sangu kwa msaada.

Nao wananchi wametumia fursa ya ziara ya mbunge Sangu kueleza kufurahishwa kwao na jitihada anazozifanya kuchangia maendeleo ya jimbo hilo ikiwemo msaada wa madawati.

Nae Bwa.Thomas Nsandale ameishukuru Ofisi ya Mbunge kwa kuwezesha wa upatikanaji wa madawati ikiwa ni miongoni mwa vingi walivyopatiwa katika kipindi chote Mhe.Sangu akiwa Mbunge wa Jimbo la Kwela

“Sangu amefanya mambo mengi ambayo yanatufanya sisi wananchi kutokupunguza upendo juu yake na tunamuomba pia Madawati haya yasiwe ya mwisho kwa wananchi wake wa Kwela Bali iwe sababu ya muendelezo wa Maendeleo haya” amesema Nsandale.

Waziri Sangu alikuwa jimboni Kwela wilaya ya Sumbawanga kukagua shughuli za maendeleo pamoja na kuzungumza na wananchi.
Na Mwandishi Wetu
BODI  ya Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC), ikiongozwa na Mwenyekiti wake, Prof. Joseph Msambichaka, imefanya ziara ya kikazi katika Bandari ya Dar es Salaam na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere (JNIA) kujionea utekelezaji wa usimamizi wa matumizi salama ya mionzi katika vifaa vya ukaguzi wa mizigo vinavyotumia teknolojia ya skana.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Prof. Msambichaka amesema Bodi imeridhishwa na kiwango cha uzingatiaji wa usalama wa mionzi pamoja na ufanisi wa matumizi ya skana katika ukaguzi wa makasha na mizigo. Amesema TAEC ina jukumu la kusimamia matumizi salama ya vifaa vinavyotumia mionzi kupitia utoaji wa leseni, ukaguzi wa mara kwa mara na mafunzo kwa watumiaji wa vifaa hivyo, ili kuhakikisha usalama wa wafanyakazi, madereva na wananchi kwa ujumla.

“Tumekuja kujionea kazi inayofanywa na TAEC katika kusimamia matumizi salama ya mionzi kwenye skana zinazotumika bandarini. Tumejiridhisha kuwa mazingira ya kazi ni salama kwa wafanyakazi, madereva na wananchi kwa ujumla,”amesema

amesema Prof. Msambichaka. Ameongeza kuwa matumizi ya teknolojia ya skana yameongeza ufanisi wa huduma bandarini kwa kupunguza muda wa ukaguzi wa makasha, kuimarisha usalama wa biashara na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa. Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Huduma za Usalama wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), Dkt. Jumanne Fhika, amesema Bandari ya Dar es Salaam kwa sasa inatumia mashine 11 za skana ambazo zimeongeza kasi na ufanisi wa ukaguzi wa mizigo, kupunguza muda wa kuhudumia makasha na kuchangia ongezeko la mapato ya Serikali. Katika kuendelea na ziara hiyo, wajumbe wa Bodi ya TAEC walitembelea eneo la ukaguzi wa mizigo katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere (JNIA), ambapo walijionea namna TAEC inavyosimamia na kudhibiti matumizi ya vifaa vya mionzi vinavyotumika kukagua mizigo inayoingia na kutoka nchini. Ziara hiyo ililenga kujiridhisha kuwa matumizi ya teknolojia ya mionzi katika ukaguzi wa mizigo yanafanyika kwa kuzingatia viwango vya usalama ili kulinda wananchi, wafanyakazi na mazingira dhidi ya athari zinazoweza kusababishwa na mionzi.

Aidha, Bodi hiyo ilitembelea Kituo cha Kitaifa cha Ufuatiliaji wa Mionzi na Uchafuzi wa Anga, kinachosimamia utekelezaji wa Mkataba wa Kupiga Marufuku Majaribio ya Silaha za Nyuklia (Comprehensive Nuclear-Test-Ban Treaty Organization – CTBTO).

Akitoa maelezo katika kituo hicho, Mkurugenzi Mkuu wa TAEC, Prof. Najat Kassim Mohammed, amesema Tanzania inaendelea kutekeleza kikamilifu wajibu wake wa kimataifa kwa kushiriki katika utekelezaji wa Mkataba wa Kupiga Marufuku Majaribio ya Silaha za Nyuklia, ikiwa ni miongoni mwa nchi zilizouridhia mkataba huo.

Prof. Najat amesema kituo hicho kina jukumu muhimu la kufuatilia na kupima viashiria vya mionzi na uchafuzi wa anga, hatua inayochangia kuimarisha usalama wa taifa, kulinda mazingira na kutekeleza wajibu wa Tanzania katika mfumo wa kimataifa wa ufuatiliaji wa majaribio ya nyuklia. Ziara hiyo imeiwezesha Bodi ya TAEC kujionea kwa karibu utekelezaji wa majukumu ya Tume katika maeneo muhimu ya kimkakati, yakiwemo usimamizi wa matumizi salama ya mionzi, ulinzi wa wananchi na mazingira, pamoja na matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika kuimarisha usalama na kuchochea maendeleo ya uchumi wa Taifa.






Na Mwandishi Wetu, Busan, Korea Kusini
KIONGOZI wa jadi wa Kimasai, Isack Lekisongo Meijo, ametoa wito wa kuwepo kwa uwiano endelevu kati ya binadamu, mifugo na wanyamapori katika Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro ili kulinda urithi huo wa dunia na kuhakikisha maendeleo endelevu ya jamii za wafugaji.

Meijo alitoa kauli hiyo wakati wa mjadala uliofanyika sambamba na Kikao cha 48 cha Kamati ya Urithi wa Dunia cha UNESCO kilichofanyika Busan, Jamhuri ya Korea, ambapo Tanzania iliwasilisha taarifa kuhusu matokeo ya Tume mbili za Rais zilizochunguza masuala ya ardhi na uhamaji wa hiari wa wananchi kutoka Ngorongoro.

Alisema kwa vizazi vingi jamii ya Wamasai imeishi sambamba na wanyamapori huku ikichangia kuhifadhi mfumo wa ikolojia wa Ngorongoro, akisisitiza kuwa hakuna Ngorongoro bila Wamasai na hakuna Ngorongoro bila wanyamapori.

Akifafanua changamoto iliyopo, Meijo alifananisha Ngorongoro na ndege inayobeba wafugaji, mifugo na wanyamapori, akisema mzigo umeongezeka kupita uwezo wa eneo hilo. Alieleza kuwa ili safari iwe salama na endelevu, ni lazima kupunguza shinikizo kwa njia iliyopangwa na yenye uwiano.

Alisema ongezeko la watu, makazi, mifugo na wanyamapori ndani ya eneo lisiloongezeka ukubwa wake limeifanya mfumo wa matumizi mchanganyiko ya ardhi kukabiliwa na changamoto kubwa za uendelevu. Kwa mujibu wake, baadhi ya wadau wanaunga mkono uhamaji wa hiari wa wafugaji kwenda maeneo yenye fursa zaidi za kijamii na kiuchumi, huku wengine wakipendekeza kuhamisha wanyamapori ili kupunguza shinikizo kwa mazingira.

Meijo alisisitiza kuwa lengo kuu ni kulinda thamani ya kipekee ya Ngorongoro kama Urithi wa Dunia huku ukiimarisha maisha ya sasa na ya baadaye ya jamii ya Wamasai. Pia aliahidi kuwa jamii hiyo itaendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania, UNESCO pamoja na wadau wengine kuhakikisha uhifadhi, utamaduni na maendeleo endelevu vinaenda sambamba.

Katika mjadala huo, mjumbe kutoka Zimbabwe alihoji ni ipi kati ya kuhamisha wafugaji au kuhamisha wanyamapori inayobeba hatari kubwa zaidi. Akijibu kwa niaba ya Serikali ya Tanzania, Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO Tanzania, Profesa Hamisi Malebo, alisema kuwa uhamaji wa hiari wa wananchi ni rahisi zaidi kuliko kuhamisha wanyamapori, jambo ambalo lina changamoto kubwa za kitaalamu, kifedha na kimazingira.

Washiriki kutoka mataifa 36 waliipongeza Tanzania kwa kuandaa mjadala huo, wakikubaliana kuwa ongezeko la watu, mifugo, migongano kati ya binadamu na wanyamapori pamoja na mabadiliko ya tabianchi vimeongeza shinikizo katika Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro na kwamba hatua za pamoja zinahitajika kulinda urithi huo wa dunia.

MAHAKAMA ya Wilaya ya Mkinga mkoani Tanga imemuhukumu Isa Musini Rashidi  maarufu kama Hamidu kifungo cha miaka 30 jela baada ya kupatikana na htia ya kosa la kusafirisha kilo 75.15 za dawa za kulevya aina ya mirungi.

Hukumu hiyo imesomwa hivi karibuni na Hakimu Mkazi Azizi Khamis, baada ya Mahakama kuridhika na ushahidi uliotolewa na upande wa mashtaka ambao uliweza kuthibitisha shtaka dhidi ya mshtakiwa bila kuacha shaka yoyote ya msingi.

Akisoma hukumu hiyo, Hakimu Khamis alisema mahakama imeridhaka na ushahidi uliowasilishwa na upande wa mashtaka na vielelezo ambapo wameweza kuthibitisha pasipo kuacha shaka yoyote kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo.

"Mahakama hii inakutia hatiani kwa kosa la kusafirisha dawa za kulevya kinyume cha Kifungu cha 16(1) na (2)(c) cha Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, Sura ya 95, Marejeo ya Mwaka 2023, na inakuhukumu kifungo cha miaka 30 jela" alisema Hakimu Khamis.

Awali mahakamani hapo ilielezwa kuwa Aprili 10, 2026, katika eneo la Kinyatu ‘A’, Wilaya ya Mkinga mkoani Tanga, maafisa wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) walimkamata Isa akiwa anaendesha pikipiki nyeusi aina ya Huoniao yenye namba za usajili MC 569 EYG, akiwa amebeba mifuko miwili iliyokuwa na jumla ya mafungu 122 ya majani yaliyodhaniwa kuwa mirungi.

Uchunguzi wa kitaalamu uliofanywa na Mkemia Mkuu wa Serikali ulithibitisha kuwa majani hayo yalikuwa mirungi yenye uzito wa kilo 75.15.

Katika kuthibitisha shtaka, upande wa mashtaka uliwasilisha mashahidi watano na vielelezo kumi huku mshtakiwa akikana tuhuma zilizokuwa zikimkabili.

Baada ya kuchambua ushahidi uliowasilishwa na pande zote, Mahakama iliridhika kuwa ushahidi wa upande wa mashtaka ulikuwa thabiti na uliweza kuthibitisha kuwa mshtakiwa alikamatwa akiwa anasafirisha mirungi hiyo.

Mahakama pia iliridhika kuwa vielelezo vilihifadhiwa na kushughulikiwa kwa kufuata taratibu, kuanzia wakati wa ukamataji, uchunguzi wa kitaalamu hadi kuharibiwa kwa mujibu wa amri ya Mahakama.

Aidha, Mahakama imeamuru pikipiki aina ya Huoniao yenye namba za usajili MC 569 EYG, iliyotumika kusafirisha dawa hizo, itaifishwe na kuuzwa kwa mnada wa hadhara.

Na Mwandishi wetu, Arusha

Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imeshiriki Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma mwaka 2026 linaloendelea jijini Arusha, limewakutanisha wadau wa ununuzi pamoja na viongozi wa Serikali kwa lengo la kujadili na kuweka mikakati ya kuimarisha Sekta ya ununuzi na ugavi nchini.

Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando, Mkuu wa Sehemu ya Huduma za Sheria PPAA, Bi. Agnes Sayi amewahimiza wadau wa ununuzi wa umma kutembelea banda la Mamlaka ya Rufani kupata uelewa juu ya majukumu na huduma mbalimbali zinazotolewa na taasisi hiyo hususan matumizi ya Moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST.

PPAA imeshiriki maonesho yanayofanyika pembezoni mwa Kongamano hilo kwa lengo la kutoa elimu kuhusu uamuzi juu ya rufaa zinazotokana na mchakato wa ununuzi wa umma, uamuzi juu ya rufaa zinazotokana na kufungiwa kushiriki katika michakato ya ununuzi wa umma pamoja na uamuzi juu ya malalamiko yanayotokana na kushindwa kwa Afisa Masuuli kutoa uamuzi ndani ya muda uliowekwa.

Awali, akifungua Kongamano hilo kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar, (Mb.), Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila amesema sekta ya ununuzi wa umma inahusisha sehemu kubwa ya matumizi ya fedha za serikali, hivyo kuna ulazima wa kuhakikisha fedha zote zinazotengwa zinasimamiwa kwa umakini mkubwa ili kuleta matokeo yaliyokusudiwa.

Dkt. Nguvila amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuimarisha matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika mfumo wa ununuzi wa umma ili kuongeza uwazi, kupunguza gharama za ununuzi, kuharakisha mchakato na kurahisisha ufuatiliaji wa matumizi ya fedha za umma.

"Ununuzi wa umma na ugavi ni nyenzo ya kisera na kimkakati ya Serikali katika kuchochea uzalishaji, ukuaji wa viwanda, kuongeza ajira, kuimarisha kampuni za ndani, kukuza ubunifu, na kuhakikisha maendeleo yanayopatikana yanawanufaisha Watanzania wengi zaidi," amesema Dkt. Nguvila.

Kongamano hilo la siku tatu limeanza tarehe 29 - 31 Julai, 2026 limewakutanisha wadau wa ununuzi zaidi ya 1,500. Aidha, limewakutanisha Wakuu wa Taasisi, Maafisa Masuuli, Maafisa Ununuzi, Idara Tumizi, Maafisa Sheria, Wazabuni na Taasisi binafsi. 





 


Mwandishi Wetu, Dar es Salaam, Julai 29, 2026

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imeanza rasmi kutoa mafunzo kwa waandishi wa habari nchini, yakilenga kuimarisha weledi, maadili na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo kwa waandishi wa habari wa Bongo FM jijini Dar es Salaam, redio dada ya Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), kwa niaba ya Mwenyekiti wa Bodi ya JAB, Tido Mhando, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, amesema mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo wa kuelewa na kutekeleza matakwa ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, kwa kuzingatia weledi, maadili na uwajibikaji.

“Mafunzo haya ni utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari. Leo tumeanza rasmi na waandishi wa habari wa Bongo FM, tutaendelea kwa vyombo vingine pia kwa sababu, kutakuwa na mafunzo ya muda mfupi na ya muda mrefu. Hivyo, mafunzo haya yawe fursa ya kujenga uwezo na kuweka msingi imara wa kukuza na kulinda taaluma ya uandishi wa habari kwa kuongeza maarifa na weledi,” amesema Wakili Kipangula.

Akiwasilisha mada kuhusu Sheria ya Huduma za Habari, historia na uanzishwaji wake, katika mafunzo hayo yaliyoanza leo tarehe 29 Julai, 2026 katika ukumbi wa Bodi, Wakili Kipangula amesema sheria hiyo imeweka msingi wa kuimarisha taaluma ya habari kwa kubainisha viwango vya weledi, maadili na uwajibikaji.

Amesisitiza kuwa JAB itaendelea kusimamia utekelezaji wa sheria hiyo kwa kuzingatia haki, uwazi na kuheshimu uhuru wa vyombo vya habari, huku ikihakikisha taaluma ya habari inalinda maslahi ya umma..

Aidha, amewataka waandishi wa habari kuzingatia sheria na maadili katika kila hatua ya ukusanyaji, uchakataji na usambazaji wa habari ili kujiepusha na madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na ukiukaji wa taaluma.

Amesema kuzingatia misingi hiyo kunajenga weledi, kunalinda heshima ya taaluma na kuimarisha imani ya jamii kwa vyombo vya habari.

Kwa upande wake, Dkt. Egbert Mkoko, akiwasilisha mada kuhusu Maadili ya Uandishi wa Habari, amesema maadili ni nguzo muhimu ya taaluma inayojengwa katika misingi ya ukweli, usahihi, haki, mizania, uwajibikaji na kutanguliza maslahi ya umma.

Amesisitiza kuwa mwandishi wa habari hapaswi kuongozwa na kasi ya kuwahi kuripoti habari, shinikizo la mitandao ya kijamii, umaarufu au maslahi binafsi, bali na ukweli na uwajibikaji.

Baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo, akiwemo Bi. Irene Kilango na Bw. Anord Philemon, wameishukuru JAB kwa kuandaa mafunzo hayo, wakisema yamewaongezea uelewa kuhusu Sheria ya Huduma za Habari, maadili ya taaluma na wajibu wa mwandishi wa habari katika kutekeleza majukumu yake kwa weledi.

"Mafunzo haya yametupatia maarifa muhimu yatakayotusaidia kutekeleza majukumu yetu kwa kuzingatia maadili, sheria na viwango vya taaluma ya uandishi wa habari. Tunaamini yatachangia kuboresha utendaji wetu na kuongeza uwajibikaji katika kuhabarisha umma," wamesema washiriki hao.

Mafunzo hayo ni sehemu ya mpango endelevu wa JAB wa kuwajengea uwezo waandishi wa habari nchini ili kuhakikisha wanazingatia Sheria ya Huduma za Habari, maadili, weledi na viwango vya taaluma katika utekelezaji wa majukumu yao, kwa lengo la kuimarisha ubora wa huduma za habari na kulinda maslahi ya umma.





Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Maonesho ya 88 ya Kitaifa ya Kilimo, Ufugaji na Uvuvi yanayotarajiwa kufungukiwa tarehe mosi  Agosti, jijini Dodoma mwaka 2026 yameweka rekodi mpya ya ushiriki wa waonyeshaji 1,133, ikiwa ni ongezeko la asilimia 26 ikilinganishwa na maonesho ya mwaka uliopita.

Washiriki hao ni pamoja na waonyeshaji 24 kutoka mataifa mbalimbali na wajasiriamali wadogo 20, hatua inayoonyesha kuendelea kukua kwa maonesho hayo na kuvutia wadau wengi wa sekta za kilimo, ufugaji na uvuvi kutoka ndani na nje ya Tanzania.

Akizungumza leo katika Viwanja vya Maonesho vya Nzuguni baada ya kukagua maandalizi ya maonesho hayo, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, amesema maandalizi yote yamekamilika na Dodoma ipo tayari kuwa mwenyeji wa maonesho hayo ya kitaifa na kimataifa.

Amesema washiriki wote wamejipanga kutoa elimu, kuonesha teknolojia za kisasa pamoja na bidhaa mbalimbali zinazohusu kilimo, uvuvi na ufugaji ili kuwawezesha wananchi kujifunza mbinu bora za kuongeza tija katika uzalishaji.

"Maonesho ya mwaka huu yamepata mwitikio mkubwa zaidi kuliko mwaka uliopita. Waonyeshaji wameongezeka kwa asilimia 26 na kufikia 1,133, jambo ambalo ni rekodi katika historia ya Viwanja vya Maonesho vya Nzuguni," amesema Senyamule.

Amewataka wananchi kutoka mikoa mbalimbali kujitokeza kutembelea maonesho hayo ili kunufaika na elimu, huduma na fursa mbalimbali zinazotolewa na taasisi za Serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo katika eneo moja.

Aidha, amesema miundombinu ya Viwanja vya Nzuguni imeendelea kuboreshwa kwa kujengwa majengo ya kisasa na ya kudumu pamoja na maeneo ya makongamano, hatua itakayowezesha uwanja huo kutumika kwa shughuli mbalimbali za kiuchumi na kijamii mwaka mzima, hata baada ya maonesho kumalizika.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Mhandisi Athumani Kilundumya, amewahamasisha Watanzania kutembelea Maonesho ya 88 ya Kitaifa pamoja na maonesho yanayofanyika katika kanda zote nane ili kujifunza teknolojia zitakazowasaidia kubadili kilimo cha mazoea na kuwa kilimo cha biashara.

Amesema matumizi ya mbegu bora bado ni changamoto kwa wakulima wengi nchini, hivyo maonesho hayo yamekusanya wataalamu mbalimbali watakaotoa elimu kuhusu mbegu bora, teknolojia za kisasa na mbinu za kuongeza uzalishaji katika sekta za kilimo, uvuvi na ufugaji.

Maonesho ya 88 Kitaifa mwaka 2026 yanatarajiwa kushirikisha wadau kutoka mataifa mbalimbali duniani, ikiwemo China, Israel, Urusi, Japan, Saudi Arabia, Sweden na nchi nyingine, huku yakitarajiwa kuwa jukwaa muhimu la kubadilishana uzoefu, teknolojia, uwekezaji na fursa za biashara katika sekta za kilimo, ufugaji na uvuvi.









 Mkuu wa mkoa wa Iringa Komred Kheri James,mapema leo amekutana na kufanya mazungumzo na viongozi wa Jumuiya za Wazee mkoani humo,lengo likiwa ni kupokea ushauri,Taarifa ya hali ya Jumuiya hizo pamoja na kushauriana juu ya masuala muhimu yanayo gusa mkoa wa Iringa.         

Akizungumza katika kikao hicho  Komred Kheri James amewashukuru Wazee wa mkoa wa Iringa kwa ushirikiano wao, busara,ushauri na ushiriki wao katika kujenga umoja,kusimamia maadili,kutoa ushauri na uzoefu,pamoja na utatuzi wa migogoro ya kijamii.                             

Aidha Komred Kheri James amewahakikishia Wazee wa mkoa wa Iringa dhamira ya Serikali kuendelea Kusimamia ustawi wa wazee,huduma kwa Wazee na kushirikiana na Jumuiya za Wazee zilizopo katika kuwahudumia na kusimamia maslahi na hoja za Wazee zinazo wasilishwa na kusimamiwa na Jumuiya hizo.









 




Na Oscar Assenga,TANGA

 Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dkt. Batilda Burian, amewataka wananchi kuacha ukataji holela wa mikoko na kushiriki kikamilifu katika uhifadhi wake, akisema misitu hiyo ni muhimu kwa kulinda fukwe, kuhifadhi viumbe wa majini na kuimarisha uchumi wa jamii za pwani.

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dkt. Batilda Burian, ameitaka jamii kuachana na tabia ya ukataji holela wa miti ya mikoko katika maeneo ya mwambao wa Bahari ya Hindi, akionya kuwa endapo vitendo hivyo vitaendelea vinaweza kuhatarisha makazi ya viumbe wa majini, maisha ya wananchi wanaotegemea rasilimali za bahari pamoja na usalama wa fukwe.

Dkt. Burian alitoa kauli hiyo Juni 28 wakati wa Maadhimisho ya Kitaifa ya Siku ya Uhifadhi wa Ikolojia ya Mikoko yaliyofanyika katika eneo la Donge Mnyanjani, Jijini Tanga. 

Alisema Mkoa wa Tanga umebarikiwa kuwa na ukanda mpana wa pwani pamoja na misitu ya mikoko yenye umuhimu mkubwa wa kiikolojia na kiuchumi katika wilaya za Mkinga, Pangani, Muheza na Jiji la Tanga.

Alieleza kuwa mikoko ni ngao muhimu inayolinda mwambao wa bahari dhidi ya mmomonyoko wa ardhi, huku pia ikiwa mazalia ya samaki na makazi ya viumbe wengine wa majini wanaochangia kuimarisha sekta ya uvuvi na kipato cha wananchi wa maeneo ya pwani.


"Mikoko ya Tanga si tu inalinda mwambao wa bahari dhidi ya mmomonyoko wa ardhi, bali ni chanzo muhimu cha maisha ya wavuvi na jamii nyingi za pwani. Kwa miaka ya hivi karibuni Mkoa wa Tanga umeendelea kuwa mfano wa uhifadhi wa mazingira unaokwenda sambamba na maendeleo ya utalii wa ikolojia," alisema Dkt. Batilda Burian.

Mkuu huyo wa Mkoa alisisitiza umuhimu wa kurejesha maeneo yaliyoharibiwa kwa kupanda mikoko mipya ili kurejesha mazingira katika hali yake ya awali kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Aidha, aliwataka viongozi wa serikali za mitaa, vikundi vya wavuvi, wanawake, vijana, wanafunzi pamoja na wadau mbalimbali wakiwemo Scouts kuendelea kushiriki kikamilifu katika juhudi za uhifadhi wa mikoko huku wakizingatia sheria na taratibu za usimamizi wa misitu.


"Tunapanda mikoko leo, lakini bado tunakabiliwa na changamoto kubwa ya uchafuzi wa mazingira unaosababishwa na mifuko ya plastiki, chupa na taka nyingine zinazotupwa ovyo kwenye fukwe zetu. Ni wajibu wetu kuendelea kutoa elimu kwa watoto na vijana kuhusu umuhimu wa kuhifadhi mikoko, kwa sababu tunapohifadhi mikoko tunalinda maisha yetu, chakula chetu, uchumi wetu na mazingira ya watoto wetu," alisisitiza Dkt. Burian.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Kamishna wa Uhifadhi kutoka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Husein Msuya, alisema Siku ya Kimataifa ya Uhifadhi wa Ikolojia ya Mikoko huadhimishwa kila mwaka ifikapo Juni 28, baada ya kuanzishwa na UNESCO mwaka 2015 kwa lengo la kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa mifumo ya ikolojia ya mikoko na wajibu wa kuihifadhi.

Alisema Tanzania ina takribani hekta 158,100 za misitu ya mikoko iliyopo katika wilaya mbalimbali za ukanda wa pwani, zikiwemo Tanga, Pangani na Mkinga, ambapo misitu hiyo ina mchango mkubwa katika kuhifadhi bioanuwai, kuzuia mmomonyoko wa fukwe, kuhifadhi kaboni na kukuza uchumi kupitia uvuvi pamoja na utalii wa ikolojia.
Wananchi wahamasisha uhifadhi wa mikoko

Mkazi wa Jiji la Tanga, Abdalah Mwalimu, alisema wananchi wana wajibu wa kutunza mikoko kwa kuwa ndiyo kinga ya kwanza dhidi ya athari za mawimbi makubwa na mabadiliko ya tabianchi yanayoathiri maeneo ya pwani.


"Mikoko ni uhai wetu. Tukiiharibu, tutakuwa tumeharibu mazalia ya samaki, tumepunguza kipato cha wavuvi na kuhatarisha usalama wa fukwe. Kila mmoja wetu anapaswa kushiriki kupanda na kuitunza," alisema Abdalah Mwalimu.

Kwa upande wake, mkazi mwingine wa Jiji la Tanga, Fatuma Omari, alisema elimu ya uhifadhi wa mazingira inapaswa kuendelea kutolewa kwa wananchi wote ili kuongeza uelewa wa umuhimu wa kupanda mikoko na kulinda fukwe.


"Kupanda mikoko ni uwekezaji wa maisha ya baadaye. Tunapaswa kuwafundisha watoto wetu kupenda mazingira ili waendeleze jukumu hili na kuhakikisha fukwe zetu zinabaki salama kwa vizazi vijavyo," alisema Fatuma Omari.

Fatuma aliongeza kuwa ushirikiano kati ya wananchi, serikali na taasisi zinazoshughulika na uhifadhi wa mazingira ni muhimu katika kuhakikisha mikoko inaendelea kulindwa na kurejeshwa katika maeneo yaliyoharibiwa.

Abdalah naye alihimiza vijana kujitokeza kwa wingi kushiriki katika kampeni za upandaji wa mikoko na usafi wa fukwe, akisema hatua hiyo itasaidia kuhifadhi mazingira, kuongeza uzalishaji wa samaki na kukuza uchumi wa jamii za pwani kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.




Na Mwandishi Wetu

MAHAKAMA ya Wilaya ya Mkinga mkoani Tanga imemhukumu Isa Musini Rashidi maarufu kama Hamidu kifungo cha miaka 30 jela baada ya kumtia hatiani kwa kosa la kusafirisha kilo 75.15 za dawa za kulevya aina ya mirungi (Khat).

Hukumu hiyo imetolewa Julai 22, 2026 na Hakimu Mkazi Azizi M. Khamis, baada ya Mahakama kuridhika kuwa upande wa mashtaka ulithibitisha shtaka dhidi ya mshtakiwa bila kuacha shaka yoyote ya msingi.

Katika kesi hiyo, Mahakama ilielezwa kuwa Aprili 10, 2026, katika eneo la Kinyatu ‘A’, Wilaya ya Mkinga mkoani Tanga, maafisa wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) walimkamata Isa akiwa anaendesha pikipiki nyeusi aina ya Huoniao yenye namba za usajili MC 569 EYG, akiwa amebeba mifuko miwili iliyokuwa na jumla ya mafungu 122 ya majani yaliyodhaniwa kuwa mirungi.

Uchunguzi wa kitaalamu uliofanywa na Mkemia Mkuu wa Serikali ulithibitisha kuwa majani hayo yalikuwa mirungi yenye uzito wa kilo 75.15.

Katika kuthibitisha shtaka, upande wa mashtaka uliwasilisha mashahidi watano na vielelezo 10, huku mshtakiwa akikana tuhuma zilizokuwa zikimkabili.

Baada ya kuchambua ushahidi uliowasilishwa na pande zote, Mahakama iliridhika kuwa ushahidi wa upande wa mashtaka ulikuwa thabiti na uliweza kuthibitisha kuwa mshtakiwa alikamatwa akiwa anasafirisha mirungi hiyo.

Mahakama pia iliridhika kuwa vielelezo vilihifadhiwa na kushughulikiwa kwa kufuata taratibu, kuanzia wakati wa ukamataji, uchunguzi wa kitaalamu hadi kuharibiwa kwa mujibu wa amri ya Mahakama.

Kwa msingi huo, Mahakama ilimtia hatiani Isa kwa kosa la kusafirisha dawa za kulevya kinyume cha Kifungu cha 16(1) na (2)(c) cha Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, Sura ya 95, Marejeo ya Mwaka 2023, na kumhukumu kifungo cha miaka 30 jela.

Aidha, Mahakama imeamuru pikipiki aina ya Huoniao yenye namba za usajili MC 569 EYG, iliyotumika kusafirisha dawa hizo, itaifishwe na kuuzwa kwa mnada wa hadhara.



 


Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Dar es Salaam imeandika historia mpya katika harakati za kuboresha huduma za afya baada ya Mkoa wa Manyara kufanikisha zoezi kubwa la kuchangisha fedha lililowezesha kupatikana kwa zaidi ya Shilingi bilioni 1.3 kwa ajili ya kuokoa maisha ya watoto wanaozaliwa njiti na kuimarisha huduma za afya katika mkoa huo.

Fedha hizo zilikusanywa kupitia hafla maalumu ya chakula cha jioni cha hisani (Manyara Tanzanite Marathon Dinner Gala) iliyofanyika Julai 24, 2026 katika Hoteli ya Serena, Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya kampeni ya Hatua Moja Okoa Maisha ya Mtoto, ambayo inalenga kuongeza upatikanaji wa vifaa tiba vya kisasa, kuboresha huduma za watoto wachanga na kupunguza vifo vinavyotokana na kuzaliwa njiti.

Jumla ya Shilingi 1,356,900,000 zilipatikana kupitia ahadi za michango na fedha taslimu kutoka kwa wadau mbalimbali wa maendeleo, taasisi za fedha, makampuni binafsi, viongozi wa Serikali, wabunge, wafanyabiashara na wananchi waliojitokeza kuunga mkono kampeni hiyo.


Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi wa kitaifa na kikanda pamoja na wadau wa sekta ya afya, ambapo mshikamano mkubwa ulionekana katika jitihada za kuhakikisha watoto wanaozaliwa njiti wanapata huduma bora na salama.

Akizungumza baada ya harambee hiyo, Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mbunge wa Babati Vijijini, Mhe. Daniel Baran Sillo, aliyekuwa mgeni rasmi, alisema mafanikio hayo yanaonesha moyo wa uzalendo na mshikamano wa Watanzania katika kusaidia sekta ya afya.

Alisema lengo la kampeni hiyo ni kufikisha zaidi ya Shilingi bilioni 1.5, huku akiwakaribisha Watanzania kushiriki Manyara Tanzanite Marathon itakayofanyika Agosti 22, 2026 mkoani Manyara.


“Tunawashukuru wadau wote waliojitokeza na kuchangia. Kila mchango una maana kubwa katika kuokoa maisha ya watoto wetu. Tunataka kuhakikisha hospitali zetu zinakuwa na vifaa vinavyohitajika kuwahudumia watoto njiti kwa kiwango cha kisasa,” alisema Mhe. Sillo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, alisema kampeni hiyo imeibuka kuwa jukwaa muhimu la kuunganisha nguvu za Serikali na sekta binafsi katika kuboresha huduma za afya kwa mama na mtoto.

Aliwataka wananchi, taasisi na wadau mbalimbali kuendelea kujitokeza kuchangia ili kufanikisha lengo lililowekwa, akisisitiza kuwa uwekezaji katika afya ya watoto ni uwekezaji katika mustakabali wa taifa.


“Kila mtoto ana haki ya kuishi. Tunapowekeza katika vifaa tiba na huduma za watoto njiti, tunaokoa familia, tunaimarisha jamii na tunajenga taifa lenye nguvu,” alisema Mhe. Sendiga.

Naye Mganga Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Dkt. Andrew Method, alieleza kuwa mkoa huo unakabiliwa na changamoto kubwa ya watoto wanaozaliwa njiti, ambapo kati ya watoto 3,000 hadi 3,200 huzaliwa njiti kila mwaka.

Alisema idadi hiyo inaweka shinikizo kubwa katika vituo vya kutolea huduma za afya, hasa katika upatikanaji wa mashine za kusaidia watoto kupumua, incubators, vifaa vya ufuatiliaji wa afya za watoto wachanga na miundombinu ya huduma maalumu.

“Watoto njiti wanahitaji uangalizi wa karibu na vifaa maalumu. Bila uwekezaji wa kutosha, tunakuwa katika hatari ya kupoteza maisha ambayo yangeweza kuokolewa,” alisema Dkt. Method.

Kwa mujibu wa wataalamu wa afya, kuzaliwa njiti ni miongoni mwa sababu kuu zinazochangia vifo vya watoto wachanga duniani, na huduma bora katika saa na siku za mwanzo baada ya kuzaliwa ndiyo huamua kwa kiasi kikubwa uwezekano wa mtoto kuendelea kuishi.

Wadau waliohudhuria hafla hiyo walieleza kuwa kampeni hiyo imeonesha mfano wa namna matukio ya michezo yanaweza kutumika kama nyenzo ya kuchangisha fedha kwa ajili ya miradi ya kijamii na maendeleo.

Mbio za Manyara Tanzanite Marathon zimekuwa zikikua kwa kasi na sasa zinatajwa kuwa moja ya matukio makubwa ya michezo na hisani nchini Tanzania, yakilenga kuhamasisha afya, utalii na maendeleo ya jamii kwa wakati mmoja.

Waandaaji wa marathon hiyo walisema fedha zitakazopatikana zitaelekezwa katika ununuzi wa vifaa tiba, uboreshaji wa huduma za watoto wachanga na kuimarisha uwezo wa hospitali za Mkoa wa Manyara kuhudumia watoto njiti kwa ufanisi zaidi.

Kampeni hiyo pia inaunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambazo zimekuwa zikilenga kuboresha huduma za afya, kupunguza vifo vya mama na mtoto, kuimarisha ustawi wa jamii na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora katika maeneo yote ya nchi.




Waandaaji wameendelea kutoa wito kwa Watanzania kushiriki mbio hizo au kuchangia kupitia akaunti maalumu za kampeni, wakisisitiza kuwa kila mchango ni hatua muhimu katika kuokoa maisha ya mtoto mmoja au zaidi.

Michango inaendelea kupokelewa kupitia CRDB Lipa Namba 113069180 na CRDB Account No. 10401215064 (Manyara Tanzania Marathon).

Kwa mafanikio yaliyopatikana katika usiku huo wa kihistoria, Mkoa wa Manyara umeonesha kuwa mshikamano wa jamii unaweza kuwa nguvu kubwa ya kuokoa maisha, huku kampeni ya Hatua Moja Okoa Maisha ya Mtoto ikiendelea kuwa mwanga wa matumaini kwa maelfu ya watoto wanaozaliwa njiti kila mwaka nchini Tanzania.




Top News