Na Janeth Raphael - MichuziTv
Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) imeweka mikakati ya muda mrefu ya kuimarisha ubora wa elimu, utafiti, ubunifu, matumizi ya TEHAMA na miundombinu, ikiwa sehemu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050 na mipango ya Serikali ya kuendeleza rasilimali watu na taasisi za elimu nchini.
Afisa Mtendaji Mkuu wa TIA, Prof. William Amos Pallangyo, amesema hayo Septemba 7, 2026, jijini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari katika Ukumbi wa Idara ya Habari – MAELEZO kuhusu utekelezaji wa shughuli za taasisi hiyo katika mwaka wa fedha 2025/26 pamoja na mwelekeo wa mwaka wa fedha 2026/27 na miaka inayofuata.
Amesema mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha mwaka wa fedha 2025/26 yameweka msingi wa TIA kuchukua hatua zaidi katika kuboresha huduma za elimu na kuongeza uwezo wa taasisi hiyo kutoa wataalamu wenye ujuzi unaokidhi mahitaji ya Taifa.
Prof. Pallangyo amesema katika mwaka wa fedha 2026/27 na miaka inayofuata, TIA itaendelea kutekeleza mipango yake kwa kuzingatia Dira ya Taifa 2050, Mpango Mkakati mpya wa TIA wa mwaka 2026/27–2030/31 pamoja na miongozo ya Serikali.
Amesema moja ya vipaumbele vya taasisi hiyo ni kuongeza ubora wa elimu kwa kuimarisha uwezo wa wahadhiri na watumishi zaidi ya 400, sambamba na kuboresha mazingira ya kujifunzia, utafiti na utoaji wa ushauri wa kitaalamu. TIA pia inalenga kuboresha maktaba na huduma za intaneti ili kuwawezesha wanafunzi na watafiti kupata nyenzo muhimu za kitaaluma kwa urahisi zaidi.
Katika hatua nyingine, taasisi hiyo inalenga kuongeza matumizi ya TEHAMA katika utoaji wa huduma kwa wanafunzi pamoja na usimamizi wa shughuli za taasisi, hatua inayotarajiwa kuongeza ufanisi na kuboresha huduma kwa wadau wake.
Kwa upande wa miundombinu, Prof. Pallangyo amesema TIA inalenga kukamilisha miradi ya kimkakati katika Kampasi za Kigoma, Mwanza, Zanzibar na Singida ili kuongeza uwezo wa taasisi hiyo kutoa huduma bora za elimu katika maeneo hayo.
Amesema TIA pia inapanga kujenga jengo jipya la taaluma katika eneo la Gezaulole, Kigamboni, kwa ajili ya kuongeza uwezo wa Kampasi ya Dar es Salaam na kupunguza msongamano uliopo katika Makao Makuu ya taasisi hiyo.
Aidha, TIA inalenga kupata eneo kwa ajili ya ujenzi wa Kampasi mpya ya Tanga, huku ikiendelea na taratibu za kukamilisha suala la fidia ya eneo lililotengwa kwa ajili ya Kampasi ya Zanzibar.
Prof. Pallangyo amesema TIA pia inaandaa mpango wa miaka 25 wa mwaka 2026 hadi 2050, ambao utaweka mwelekeo wa muda mrefu wa taasisi hiyo katika maeneo mbalimbali ya kimkakati, yakiwemo elimu, utafiti, ubunifu, TEHAMA, miundombinu na ushirikiano wa kimataifa.
Amesema mpango huo utaendana na Dira ya Taifa 2050 pamoja na Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2025–2030, kwa lengo la kuhakikisha TIA inaendelea kujenga uwezo wa kitaaluma na kuzalisha wataalamu watakaokuwa na mchango katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii ya Tanzania.
“Mafanikio haya yanaweka msingi wa hatua nyingine kubwa zaidi,” amesema Prof. Pallangyo, akieleza kuwa TIA itaendelea kuchukua hatua za kimkakati katika kuimarisha elimu, utafiti na huduma zake ili kuendana na mahitaji ya Taifa katika safari ya kuelekea mwaka 2050.




.jpeg)


.jpeg)






.jpeg)


.jpeg)
.jpeg)





.jpeg)










.jpeg)


.jpeg)


.jpeg)

.jpeg)



