Mwandishi Wetu, Dar es Salaam, Julai 29, 2026

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imeanza rasmi kutoa mafunzo kwa waandishi wa habari nchini, yakilenga kuimarisha weledi, maadili na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo kwa waandishi wa habari wa Bongo FM jijini Dar es Salaam, redio dada ya Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), kwa niaba ya Mwenyekiti wa Bodi ya JAB, Tido Mhando, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, amesema mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo wa kuelewa na kutekeleza matakwa ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, kwa kuzingatia weledi, maadili na uwajibikaji.

“Mafunzo haya ni utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari. Leo tumeanza rasmi na waandishi wa habari wa Bongo FM, tutaendelea kwa vyombo vingine pia kwa sababu, kutakuwa na mafunzo ya muda mfupi na ya muda mrefu. Hivyo, mafunzo haya yawe fursa ya kujenga uwezo na kuweka msingi imara wa kukuza na kulinda taaluma ya uandishi wa habari kwa kuongeza maarifa na weledi,” amesema Wakili Kipangula.

Akiwasilisha mada kuhusu Sheria ya Huduma za Habari, historia na uanzishwaji wake, katika mafunzo hayo yaliyoanza leo tarehe 29 Julai, 2026 katika ukumbi wa Bodi, Wakili Kipangula amesema sheria hiyo imeweka msingi wa kuimarisha taaluma ya habari kwa kubainisha viwango vya weledi, maadili na uwajibikaji.

Amesisitiza kuwa JAB itaendelea kusimamia utekelezaji wa sheria hiyo kwa kuzingatia haki, uwazi na kuheshimu uhuru wa vyombo vya habari, huku ikihakikisha taaluma ya habari inalinda maslahi ya umma..

Aidha, amewataka waandishi wa habari kuzingatia sheria na maadili katika kila hatua ya ukusanyaji, uchakataji na usambazaji wa habari ili kujiepusha na madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na ukiukaji wa taaluma.

Amesema kuzingatia misingi hiyo kunajenga weledi, kunalinda heshima ya taaluma na kuimarisha imani ya jamii kwa vyombo vya habari.

Kwa upande wake, Dkt. Egbert Mkoko, akiwasilisha mada kuhusu Maadili ya Uandishi wa Habari, amesema maadili ni nguzo muhimu ya taaluma inayojengwa katika misingi ya ukweli, usahihi, haki, mizania, uwajibikaji na kutanguliza maslahi ya umma.

Amesisitiza kuwa mwandishi wa habari hapaswi kuongozwa na kasi ya kuwahi kuripoti habari, shinikizo la mitandao ya kijamii, umaarufu au maslahi binafsi, bali na ukweli na uwajibikaji.

Baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo, akiwemo Bi. Irene Kilango na Bw. Anord Philemon, wameishukuru JAB kwa kuandaa mafunzo hayo, wakisema yamewaongezea uelewa kuhusu Sheria ya Huduma za Habari, maadili ya taaluma na wajibu wa mwandishi wa habari katika kutekeleza majukumu yake kwa weledi.

"Mafunzo haya yametupatia maarifa muhimu yatakayotusaidia kutekeleza majukumu yetu kwa kuzingatia maadili, sheria na viwango vya taaluma ya uandishi wa habari. Tunaamini yatachangia kuboresha utendaji wetu na kuongeza uwajibikaji katika kuhabarisha umma," wamesema washiriki hao.

Mafunzo hayo ni sehemu ya mpango endelevu wa JAB wa kuwajengea uwezo waandishi wa habari nchini ili kuhakikisha wanazingatia Sheria ya Huduma za Habari, maadili, weledi na viwango vya taaluma katika utekelezaji wa majukumu yao, kwa lengo la kuimarisha ubora wa huduma za habari na kulinda maslahi ya umma.





Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Maonesho ya 88 ya Kitaifa ya Kilimo, Ufugaji na Uvuvi yanayotarajiwa kufungukiwa tarehe mosi  Agosti, jijini Dodoma mwaka 2026 yameweka rekodi mpya ya ushiriki wa waonyeshaji 1,133, ikiwa ni ongezeko la asilimia 26 ikilinganishwa na maonesho ya mwaka uliopita.

Washiriki hao ni pamoja na waonyeshaji 24 kutoka mataifa mbalimbali na wajasiriamali wadogo 20, hatua inayoonyesha kuendelea kukua kwa maonesho hayo na kuvutia wadau wengi wa sekta za kilimo, ufugaji na uvuvi kutoka ndani na nje ya Tanzania.

Akizungumza leo katika Viwanja vya Maonesho vya Nzuguni baada ya kukagua maandalizi ya maonesho hayo, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, amesema maandalizi yote yamekamilika na Dodoma ipo tayari kuwa mwenyeji wa maonesho hayo ya kitaifa na kimataifa.

Amesema washiriki wote wamejipanga kutoa elimu, kuonesha teknolojia za kisasa pamoja na bidhaa mbalimbali zinazohusu kilimo, uvuvi na ufugaji ili kuwawezesha wananchi kujifunza mbinu bora za kuongeza tija katika uzalishaji.

"Maonesho ya mwaka huu yamepata mwitikio mkubwa zaidi kuliko mwaka uliopita. Waonyeshaji wameongezeka kwa asilimia 26 na kufikia 1,133, jambo ambalo ni rekodi katika historia ya Viwanja vya Maonesho vya Nzuguni," amesema Senyamule.

Amewataka wananchi kutoka mikoa mbalimbali kujitokeza kutembelea maonesho hayo ili kunufaika na elimu, huduma na fursa mbalimbali zinazotolewa na taasisi za Serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo katika eneo moja.

Aidha, amesema miundombinu ya Viwanja vya Nzuguni imeendelea kuboreshwa kwa kujengwa majengo ya kisasa na ya kudumu pamoja na maeneo ya makongamano, hatua itakayowezesha uwanja huo kutumika kwa shughuli mbalimbali za kiuchumi na kijamii mwaka mzima, hata baada ya maonesho kumalizika.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Mhandisi Athumani Kilundumya, amewahamasisha Watanzania kutembelea Maonesho ya 88 ya Kitaifa pamoja na maonesho yanayofanyika katika kanda zote nane ili kujifunza teknolojia zitakazowasaidia kubadili kilimo cha mazoea na kuwa kilimo cha biashara.

Amesema matumizi ya mbegu bora bado ni changamoto kwa wakulima wengi nchini, hivyo maonesho hayo yamekusanya wataalamu mbalimbali watakaotoa elimu kuhusu mbegu bora, teknolojia za kisasa na mbinu za kuongeza uzalishaji katika sekta za kilimo, uvuvi na ufugaji.

Maonesho ya 88 Kitaifa mwaka 2026 yanatarajiwa kushirikisha wadau kutoka mataifa mbalimbali duniani, ikiwemo China, Israel, Urusi, Japan, Saudi Arabia, Sweden na nchi nyingine, huku yakitarajiwa kuwa jukwaa muhimu la kubadilishana uzoefu, teknolojia, uwekezaji na fursa za biashara katika sekta za kilimo, ufugaji na uvuvi.









 Mkuu wa mkoa wa Iringa Komred Kheri James,mapema leo amekutana na kufanya mazungumzo na viongozi wa Jumuiya za Wazee mkoani humo,lengo likiwa ni kupokea ushauri,Taarifa ya hali ya Jumuiya hizo pamoja na kushauriana juu ya masuala muhimu yanayo gusa mkoa wa Iringa.         

Akizungumza katika kikao hicho  Komred Kheri James amewashukuru Wazee wa mkoa wa Iringa kwa ushirikiano wao, busara,ushauri na ushiriki wao katika kujenga umoja,kusimamia maadili,kutoa ushauri na uzoefu,pamoja na utatuzi wa migogoro ya kijamii.                             

Aidha Komred Kheri James amewahakikishia Wazee wa mkoa wa Iringa dhamira ya Serikali kuendelea Kusimamia ustawi wa wazee,huduma kwa Wazee na kushirikiana na Jumuiya za Wazee zilizopo katika kuwahudumia na kusimamia maslahi na hoja za Wazee zinazo wasilishwa na kusimamiwa na Jumuiya hizo.









 




Na Oscar Assenga,TANGA

 Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dkt. Batilda Burian, amewataka wananchi kuacha ukataji holela wa mikoko na kushiriki kikamilifu katika uhifadhi wake, akisema misitu hiyo ni muhimu kwa kulinda fukwe, kuhifadhi viumbe wa majini na kuimarisha uchumi wa jamii za pwani.

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dkt. Batilda Burian, ameitaka jamii kuachana na tabia ya ukataji holela wa miti ya mikoko katika maeneo ya mwambao wa Bahari ya Hindi, akionya kuwa endapo vitendo hivyo vitaendelea vinaweza kuhatarisha makazi ya viumbe wa majini, maisha ya wananchi wanaotegemea rasilimali za bahari pamoja na usalama wa fukwe.

Dkt. Burian alitoa kauli hiyo Juni 28 wakati wa Maadhimisho ya Kitaifa ya Siku ya Uhifadhi wa Ikolojia ya Mikoko yaliyofanyika katika eneo la Donge Mnyanjani, Jijini Tanga. 

Alisema Mkoa wa Tanga umebarikiwa kuwa na ukanda mpana wa pwani pamoja na misitu ya mikoko yenye umuhimu mkubwa wa kiikolojia na kiuchumi katika wilaya za Mkinga, Pangani, Muheza na Jiji la Tanga.

Alieleza kuwa mikoko ni ngao muhimu inayolinda mwambao wa bahari dhidi ya mmomonyoko wa ardhi, huku pia ikiwa mazalia ya samaki na makazi ya viumbe wengine wa majini wanaochangia kuimarisha sekta ya uvuvi na kipato cha wananchi wa maeneo ya pwani.


"Mikoko ya Tanga si tu inalinda mwambao wa bahari dhidi ya mmomonyoko wa ardhi, bali ni chanzo muhimu cha maisha ya wavuvi na jamii nyingi za pwani. Kwa miaka ya hivi karibuni Mkoa wa Tanga umeendelea kuwa mfano wa uhifadhi wa mazingira unaokwenda sambamba na maendeleo ya utalii wa ikolojia," alisema Dkt. Batilda Burian.

Mkuu huyo wa Mkoa alisisitiza umuhimu wa kurejesha maeneo yaliyoharibiwa kwa kupanda mikoko mipya ili kurejesha mazingira katika hali yake ya awali kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Aidha, aliwataka viongozi wa serikali za mitaa, vikundi vya wavuvi, wanawake, vijana, wanafunzi pamoja na wadau mbalimbali wakiwemo Scouts kuendelea kushiriki kikamilifu katika juhudi za uhifadhi wa mikoko huku wakizingatia sheria na taratibu za usimamizi wa misitu.


"Tunapanda mikoko leo, lakini bado tunakabiliwa na changamoto kubwa ya uchafuzi wa mazingira unaosababishwa na mifuko ya plastiki, chupa na taka nyingine zinazotupwa ovyo kwenye fukwe zetu. Ni wajibu wetu kuendelea kutoa elimu kwa watoto na vijana kuhusu umuhimu wa kuhifadhi mikoko, kwa sababu tunapohifadhi mikoko tunalinda maisha yetu, chakula chetu, uchumi wetu na mazingira ya watoto wetu," alisisitiza Dkt. Burian.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Kamishna wa Uhifadhi kutoka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Husein Msuya, alisema Siku ya Kimataifa ya Uhifadhi wa Ikolojia ya Mikoko huadhimishwa kila mwaka ifikapo Juni 28, baada ya kuanzishwa na UNESCO mwaka 2015 kwa lengo la kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa mifumo ya ikolojia ya mikoko na wajibu wa kuihifadhi.

Alisema Tanzania ina takribani hekta 158,100 za misitu ya mikoko iliyopo katika wilaya mbalimbali za ukanda wa pwani, zikiwemo Tanga, Pangani na Mkinga, ambapo misitu hiyo ina mchango mkubwa katika kuhifadhi bioanuwai, kuzuia mmomonyoko wa fukwe, kuhifadhi kaboni na kukuza uchumi kupitia uvuvi pamoja na utalii wa ikolojia.
Wananchi wahamasisha uhifadhi wa mikoko

Mkazi wa Jiji la Tanga, Abdalah Mwalimu, alisema wananchi wana wajibu wa kutunza mikoko kwa kuwa ndiyo kinga ya kwanza dhidi ya athari za mawimbi makubwa na mabadiliko ya tabianchi yanayoathiri maeneo ya pwani.


"Mikoko ni uhai wetu. Tukiiharibu, tutakuwa tumeharibu mazalia ya samaki, tumepunguza kipato cha wavuvi na kuhatarisha usalama wa fukwe. Kila mmoja wetu anapaswa kushiriki kupanda na kuitunza," alisema Abdalah Mwalimu.

Kwa upande wake, mkazi mwingine wa Jiji la Tanga, Fatuma Omari, alisema elimu ya uhifadhi wa mazingira inapaswa kuendelea kutolewa kwa wananchi wote ili kuongeza uelewa wa umuhimu wa kupanda mikoko na kulinda fukwe.


"Kupanda mikoko ni uwekezaji wa maisha ya baadaye. Tunapaswa kuwafundisha watoto wetu kupenda mazingira ili waendeleze jukumu hili na kuhakikisha fukwe zetu zinabaki salama kwa vizazi vijavyo," alisema Fatuma Omari.

Fatuma aliongeza kuwa ushirikiano kati ya wananchi, serikali na taasisi zinazoshughulika na uhifadhi wa mazingira ni muhimu katika kuhakikisha mikoko inaendelea kulindwa na kurejeshwa katika maeneo yaliyoharibiwa.

Abdalah naye alihimiza vijana kujitokeza kwa wingi kushiriki katika kampeni za upandaji wa mikoko na usafi wa fukwe, akisema hatua hiyo itasaidia kuhifadhi mazingira, kuongeza uzalishaji wa samaki na kukuza uchumi wa jamii za pwani kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.




Na Mwandishi Wetu

MAHAKAMA ya Wilaya ya Mkinga mkoani Tanga imemhukumu Isa Musini Rashidi maarufu kama Hamidu kifungo cha miaka 30 jela baada ya kumtia hatiani kwa kosa la kusafirisha kilo 75.15 za dawa za kulevya aina ya mirungi (Khat).

Hukumu hiyo imetolewa Julai 22, 2026 na Hakimu Mkazi Azizi M. Khamis, baada ya Mahakama kuridhika kuwa upande wa mashtaka ulithibitisha shtaka dhidi ya mshtakiwa bila kuacha shaka yoyote ya msingi.

Katika kesi hiyo, Mahakama ilielezwa kuwa Aprili 10, 2026, katika eneo la Kinyatu ‘A’, Wilaya ya Mkinga mkoani Tanga, maafisa wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) walimkamata Isa akiwa anaendesha pikipiki nyeusi aina ya Huoniao yenye namba za usajili MC 569 EYG, akiwa amebeba mifuko miwili iliyokuwa na jumla ya mafungu 122 ya majani yaliyodhaniwa kuwa mirungi.

Uchunguzi wa kitaalamu uliofanywa na Mkemia Mkuu wa Serikali ulithibitisha kuwa majani hayo yalikuwa mirungi yenye uzito wa kilo 75.15.

Katika kuthibitisha shtaka, upande wa mashtaka uliwasilisha mashahidi watano na vielelezo 10, huku mshtakiwa akikana tuhuma zilizokuwa zikimkabili.

Baada ya kuchambua ushahidi uliowasilishwa na pande zote, Mahakama iliridhika kuwa ushahidi wa upande wa mashtaka ulikuwa thabiti na uliweza kuthibitisha kuwa mshtakiwa alikamatwa akiwa anasafirisha mirungi hiyo.

Mahakama pia iliridhika kuwa vielelezo vilihifadhiwa na kushughulikiwa kwa kufuata taratibu, kuanzia wakati wa ukamataji, uchunguzi wa kitaalamu hadi kuharibiwa kwa mujibu wa amri ya Mahakama.

Kwa msingi huo, Mahakama ilimtia hatiani Isa kwa kosa la kusafirisha dawa za kulevya kinyume cha Kifungu cha 16(1) na (2)(c) cha Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, Sura ya 95, Marejeo ya Mwaka 2023, na kumhukumu kifungo cha miaka 30 jela.

Aidha, Mahakama imeamuru pikipiki aina ya Huoniao yenye namba za usajili MC 569 EYG, iliyotumika kusafirisha dawa hizo, itaifishwe na kuuzwa kwa mnada wa hadhara.



 


Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Dar es Salaam imeandika historia mpya katika harakati za kuboresha huduma za afya baada ya Mkoa wa Manyara kufanikisha zoezi kubwa la kuchangisha fedha lililowezesha kupatikana kwa zaidi ya Shilingi bilioni 1.3 kwa ajili ya kuokoa maisha ya watoto wanaozaliwa njiti na kuimarisha huduma za afya katika mkoa huo.

Fedha hizo zilikusanywa kupitia hafla maalumu ya chakula cha jioni cha hisani (Manyara Tanzanite Marathon Dinner Gala) iliyofanyika Julai 24, 2026 katika Hoteli ya Serena, Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya kampeni ya Hatua Moja Okoa Maisha ya Mtoto, ambayo inalenga kuongeza upatikanaji wa vifaa tiba vya kisasa, kuboresha huduma za watoto wachanga na kupunguza vifo vinavyotokana na kuzaliwa njiti.

Jumla ya Shilingi 1,356,900,000 zilipatikana kupitia ahadi za michango na fedha taslimu kutoka kwa wadau mbalimbali wa maendeleo, taasisi za fedha, makampuni binafsi, viongozi wa Serikali, wabunge, wafanyabiashara na wananchi waliojitokeza kuunga mkono kampeni hiyo.


Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi wa kitaifa na kikanda pamoja na wadau wa sekta ya afya, ambapo mshikamano mkubwa ulionekana katika jitihada za kuhakikisha watoto wanaozaliwa njiti wanapata huduma bora na salama.

Akizungumza baada ya harambee hiyo, Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mbunge wa Babati Vijijini, Mhe. Daniel Baran Sillo, aliyekuwa mgeni rasmi, alisema mafanikio hayo yanaonesha moyo wa uzalendo na mshikamano wa Watanzania katika kusaidia sekta ya afya.

Alisema lengo la kampeni hiyo ni kufikisha zaidi ya Shilingi bilioni 1.5, huku akiwakaribisha Watanzania kushiriki Manyara Tanzanite Marathon itakayofanyika Agosti 22, 2026 mkoani Manyara.


“Tunawashukuru wadau wote waliojitokeza na kuchangia. Kila mchango una maana kubwa katika kuokoa maisha ya watoto wetu. Tunataka kuhakikisha hospitali zetu zinakuwa na vifaa vinavyohitajika kuwahudumia watoto njiti kwa kiwango cha kisasa,” alisema Mhe. Sillo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, alisema kampeni hiyo imeibuka kuwa jukwaa muhimu la kuunganisha nguvu za Serikali na sekta binafsi katika kuboresha huduma za afya kwa mama na mtoto.

Aliwataka wananchi, taasisi na wadau mbalimbali kuendelea kujitokeza kuchangia ili kufanikisha lengo lililowekwa, akisisitiza kuwa uwekezaji katika afya ya watoto ni uwekezaji katika mustakabali wa taifa.


“Kila mtoto ana haki ya kuishi. Tunapowekeza katika vifaa tiba na huduma za watoto njiti, tunaokoa familia, tunaimarisha jamii na tunajenga taifa lenye nguvu,” alisema Mhe. Sendiga.

Naye Mganga Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Dkt. Andrew Method, alieleza kuwa mkoa huo unakabiliwa na changamoto kubwa ya watoto wanaozaliwa njiti, ambapo kati ya watoto 3,000 hadi 3,200 huzaliwa njiti kila mwaka.

Alisema idadi hiyo inaweka shinikizo kubwa katika vituo vya kutolea huduma za afya, hasa katika upatikanaji wa mashine za kusaidia watoto kupumua, incubators, vifaa vya ufuatiliaji wa afya za watoto wachanga na miundombinu ya huduma maalumu.

“Watoto njiti wanahitaji uangalizi wa karibu na vifaa maalumu. Bila uwekezaji wa kutosha, tunakuwa katika hatari ya kupoteza maisha ambayo yangeweza kuokolewa,” alisema Dkt. Method.

Kwa mujibu wa wataalamu wa afya, kuzaliwa njiti ni miongoni mwa sababu kuu zinazochangia vifo vya watoto wachanga duniani, na huduma bora katika saa na siku za mwanzo baada ya kuzaliwa ndiyo huamua kwa kiasi kikubwa uwezekano wa mtoto kuendelea kuishi.

Wadau waliohudhuria hafla hiyo walieleza kuwa kampeni hiyo imeonesha mfano wa namna matukio ya michezo yanaweza kutumika kama nyenzo ya kuchangisha fedha kwa ajili ya miradi ya kijamii na maendeleo.

Mbio za Manyara Tanzanite Marathon zimekuwa zikikua kwa kasi na sasa zinatajwa kuwa moja ya matukio makubwa ya michezo na hisani nchini Tanzania, yakilenga kuhamasisha afya, utalii na maendeleo ya jamii kwa wakati mmoja.

Waandaaji wa marathon hiyo walisema fedha zitakazopatikana zitaelekezwa katika ununuzi wa vifaa tiba, uboreshaji wa huduma za watoto wachanga na kuimarisha uwezo wa hospitali za Mkoa wa Manyara kuhudumia watoto njiti kwa ufanisi zaidi.

Kampeni hiyo pia inaunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambazo zimekuwa zikilenga kuboresha huduma za afya, kupunguza vifo vya mama na mtoto, kuimarisha ustawi wa jamii na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora katika maeneo yote ya nchi.




Waandaaji wameendelea kutoa wito kwa Watanzania kushiriki mbio hizo au kuchangia kupitia akaunti maalumu za kampeni, wakisisitiza kuwa kila mchango ni hatua muhimu katika kuokoa maisha ya mtoto mmoja au zaidi.

Michango inaendelea kupokelewa kupitia CRDB Lipa Namba 113069180 na CRDB Account No. 10401215064 (Manyara Tanzania Marathon).

Kwa mafanikio yaliyopatikana katika usiku huo wa kihistoria, Mkoa wa Manyara umeonesha kuwa mshikamano wa jamii unaweza kuwa nguvu kubwa ya kuokoa maisha, huku kampeni ya Hatua Moja Okoa Maisha ya Mtoto ikiendelea kuwa mwanga wa matumaini kwa maelfu ya watoto wanaozaliwa njiti kila mwaka nchini Tanzania.




Top News