DODOMA | 24 Julai 2026

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro, amekutana na Wabunge wa Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA) kutoka Tanzania Makao Makuu ya CCM, Dodoma, na kuwapongeza kwa dhamana ya kuiwakilisha nchi katika chombo hicho cha kikanda.

Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika leo Julai 24,2026, Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro,amewahimiza kuendelea kutanguliza maslahi ya Taifa na Jumuiya kwa kudumisha mshikamano, kujenga ushirikiano na wabunge kutoka nchi wanachama katika kuimarisha mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ambao Tanzania inajivunia kuwa moja wa waasisi wake.

Katibu Mkuu amesisitiza kuwa Chama kina matarajio makubwa kwao na kitaendelea kuwapa ushirikiano wanapotekeleza wajibu wao wa kitaifa na kikanda.
NA DENIS MLOWE, IRINGA

MBUNGE wa Viti Maalum Mkoa wa Iringa, Nancy Nyalusi, amesema ujenzi wa jengo jipya la Mama na Mtoto ni hatua muhimu katika kuboresha huduma za afya na unatarajiwa kupunguza vifo vya wajawazito na watoto wachanga huku ukiimarisha upatikanaji wa huduma bora kwa wananchi wa Mkoa wa Iringa.

Nyalusi alitoa kauli hiyo wakati wa uzinduzi wa jengo hilo uliohudhuriwa na Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, ambapo alimkaribisha wilayani Iringa na kueleza kuwa wananchi wa mkoa huo wanaendelea kushuhudia matokeo makubwa ya uwekezaji wa Serikali katika sekta mbalimbali za maendeleo.

Alisema Serikali imeendelea kuonyesha dhamira ya dhati ya kuboresha sekta ya afya kwa kujenga miundombinu ya kisasa inayowezesha wananchi kupata huduma bora karibu na maeneo yao.

"Jengo hili la Mama na Mtoto litasaidia kupunguza vifo vya akina mama na watoto wachanga, huku likiboresha mazingira ya utoaji wa huduma za afya hivyo tunamshukuru sana Rais na Serikali kwa kuendelea kutuletea miradi ya maendeleo inayogusa maisha ya wananchi," alisema Nyalusi.

Nyalusi alisema kuwa uwekezaji unaofanywa katika sekta ya afya umeongeza matumaini kwa wananchi, hasa wanawake na watoto ambao ndio wanufaika wakuu wa huduma hizo.

Pia aliwataka wananchi kutunza miundombinu hiyo ili iweze kuendelea kutoa huduma kwa ufanisi kwa miaka mingi ijayo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Kheri James, alisema ujio wa Waziri wa Ujenzi ni fursa kwa Serikali kujionea hatua kubwa ambazo Mkoa wa Iringa umezipiga katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Alisema uwepo wa Waziri huyo ni ishara ya namna Serikali ya Rais inavyofuatilia kwa karibu maendeleo ya miradi ya umma na kuhakikisha uwekezaji unaofanywa unaleta matokeo yaliyokusudiwa.

"Leo tumepata nafasi ya jicho la Mheshimiwa Rais kupitia Waziri wa Ujenzi mh Ulega kuona ni kwa kiwango gani tumepiga hatua kama wana Iringa," alisema Kheri.

James aliipongeza Halmashauri ya Manispaa ya Iringa kwa maandalizi mazuri ya hafla hiyo, akisema yameonyesha uwezo wa mkoa katika kupokea wageni wa kitaifa na kusimamia shughuli za maendeleo.

Aidha, aliisifu Hospitali ya Manispaa ya Iringa kwa ubora wa huduma zinazotolewa na watumishi wake, akieleza kuwa hospitali hiyo imekuwa mfano wa utoaji wa huduma zenye utu na kuwapa wagonjwa faraja tangu wanapowasili.

"Hii ni miongoni mwa hospitali zenye watumishi bora sana. Hapa tuna wahudumu wazuri ambao hata kabla hawajakupa dawa, maneno yao yanawafariji wagonjwa. Kuanzia mapokezi namna wananchi wanavyopokelewa, jambo hilo linatia moyo sana," alisema.

Kheri alisema mafanikio ya sekta ya afya hayategemei ujenzi wa majengo pekee bali pia yanahitaji watumishi wenye weledi, maadili na moyo wa kuwahudumia wananchi kwa upendo

Uzinduzi wa ujenzi wa jengo hilo la Mama na Mtoto unatajwa kuwa sehemu ya jitihada za Serikali za kuendelea kuboresha huduma za afya nchini kwa kujenga miundombinu ya kisasa,kuongeza ubora wa huduma na kupunguza vifo vinavyoweza kuzuilika kwa akina mama na watoto wachanga, huku wananchi wa Mkoa wa Iringa wakieleza matumaini makubwa kuwa huduma zitaboreshwa zaidi baada ya kuanza kutumika kwa jengo hilo.






Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amesema ikiwa angepewa nafasi ya kutoa ujumbe mmoja wa mwisho kwa Watanzania, basi usingekuwa mwingine zaidi ya kuwahimiza kuendelea kupambana kwa ajili ya kupata Katiba Mpya itakayokuwa na mwafaka wa kitaifa na kudumu kwa angalau miaka 50 ijayo.

Dkt. Nchimbi ametoa kauli hiyo leo  jijini Dar es Salaam alipokuwa akizungumza katika Mkutano Mkuu wa Wanachama wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu, ambapo alizungumzia historia ya safari ya Tanzania kuelekea kupata Katiba Mpya na umuhimu wa kuendelea kujenga maridhiano katika mchakato huo.

Amesema mjadala kuhusu Katiba Mpya si wa leo wala wa jana, bali ni ajenda ambayo imeendelea kujadiliwa kwa zaidi ya miongo minne, huku akieleza kuwa vuguvugu la kuisukuma kwa nguvu lilianza mwaka 1992 baada ya kurejeshwa kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa.

Kwa mujibu wa Makamu wa Rais, Tanzania imepitia hatua mbalimbali katika kutafuta Katiba Mpya, ikiwemo juhudi zilizofanywa na Serikali ya Awamu ya Nne iliyoanzisha rasmi mchakato wa kuandaa Katiba hiyo. Hata hivyo, alisema mchakato huo ulikumbana na changamoto mbalimbali kutokana na wingi wa maoni, matarajio na mahitaji yaliyowasilishwa na wananchi kutoka maeneo tofauti ya nchi.

Ameeleza kuwa Katiba ni msingi mkuu wa uongozi na maendeleo ya Taifa, hivyo inahitaji kujengwa kwa maridhiano mapana yatakayowakutanisha Watanzania wenye mitazamo tofauti kwa lengo la kuweka mbele maslahi ya Taifa badala ya maslahi binafsi au ya kisiasa.

Dkt. Nchimbi amesema mafanikio ya mchakato wa Katiba Mpya yatategemea uwezo wa Watanzania kuendelea kushiriki kwa uwazi, kuheshimiana na kujenga makubaliano yatakayozalisha Katiba imara, ya kisasa na inayokidhi mahitaji ya kizazi cha sasa pamoja na vizazi vijavyo.

"Kama nina kitu cha kuwaambia Watanzania, ningewaambia pambaneni mpate Katiba Mpya itakayodumu miaka 50, yenye mwafaka katika Taifa, itakayotupeleka mbele miaka 50," amesema Dkt. Nchimbi.

Ameongeza kuwa lengo la Katiba Mpya halipaswi kuwa kushinda au kushindwa kwa upande mmoja, bali kujenga msingi wa umoja, utulivu, haki na maendeleo endelevu ya Taifa kwa muda mrefu.

Kauli hiyo ya Makamu wa Rais imekuja wakati ambapo mjadala kuhusu mustakabali wa mchakato wa Katiba Mpya unaendelea kujitokeza katika maeneo mbalimbali nchini, huku wadau wa haki za binadamu, asasi za kiraia, viongozi wa dini, vyama vya siasa na makundi mengine ya kijamii wakiendelea kusisitiza umuhimu wa maridhiano na ushirikishwaji mpana wa wananchi katika kufikia Katiba inayokubalika na Watanzania wote.







Na Mwandishi Wetu


KAMPUNI ya Oryx Gas imekabidhi mitungi ya gesi ya kupikia 600 kwa makundi mbalimbali ya wajasiriamali wakimo mama lishe huku Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo Subira Mgalu akieleza kuwa uamuzi wa Oryx kugawa mitungi hiyo kunakwenda kuondoa kabisa athari za kiafya zinazotokana na matumizi ya nishati chafu kama kuni na mkaa.

Mgalu ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge na Nishati na Madini ameyasema hayo leo Julai 24,2026 katika Tamasha la Samaki wilayani Bagamoyo ambapo kupitia tamasha hilo limetumika kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia ambapo yametolewa pia mafunzo ya matumizi salama ya nishati hiyo.

“Oryx Gas wamekuwa wadau wakubwa katika kuhamasisha nishati safi ya kupikia ya gesi ya LPG kwa vitendo na kupitia Samaki Festival wameamua kuunga mkono juhudi za Serikali kwa kugawa mitungi ya gesi kwa makundi mbalimbali yakiwemo ya Mama

Na Baba Lishe na wafanyabiashara wa soko la Samaki Bagamoyo.

“Tunafahamu kabla ya Serikali inayoongozwa na Rais Dk.Samia Suluhu Hassan ambaye ni kinara wa nishati Afrika kuja na kampeni ya nishati safi ya kupikia kulikuwa na matumizi makubwa ya kuni na mkaa hali iliyosababisha watumiaji wa nishati hiyo kuwa na athari za kiafya huku watu 32,000 wakipoteza maisha kutokana na madhara ya kutumia kuni na mkaa,”amesema Mgalu.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Oryx Energies Tanzania Imani Mtafya amesema katika kuunga mkono juhudi za Serikali kuhamasisha nishati safi ya kupikia wamekabidhi mitungi ya gesi 600 yenye thamani ya Sh.milioni 48 kwa makundi mbalimbali ya wajasiriamali.

Pia amesema kuanzia mwaka 2021 hadi mwaka 2026 wameshatoa mitungi 72000 yenye thamani ya Sh.bilioni 5.7 , lengo likiwa kuunga mkono juhudi za Serikali ambayo imeweka lengo ifikapo 2034 watumiaji wa nishati safi ya kupikia wawe wamefikia asilimia 80 kutoka asilimia 29 iliyopo sasa .

Mtafya amesema juhudi wanazofanya zinalenga pia kukomesha utumiaji wa kuni na mkaa ambao unaathiri kubwa sio tu kwa mazingira lakini kwa afya ya mtumiaji huku akifafanua kwasasa wanafanya uwekezaji mkubwa ili kuendana na sera ya Serikali ya kuhamasisha nishati safi ya kupikia.

“Tumewekeza katika ujenzi wa miundombinu ya ghala jipya la kuhifadhi gesi ambalo litagharimu Sh.bilioni 40 ili kuhakikisha tunaongeza usambazaji wetu wa gesi nchi nzima.”

Wakati huo huo Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani Shaibu Ndemanga aliyekuwa mgeni rasmi katika Tamasha la Samaki ametumia nafasi hiyo kuelezea mkakati wao katika kuhamasisha nishati safi ya kupikia na kwamba uamuzi wa Oryx Gas kugawa mitungi 600 ni hatua inayoonesha dhamira ya kuachana na kuni na mkaa hasa kwa wakaanga Samaki wa Soko la Bagamoyo .









 Naibu Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile, Julai 24, akipata maelezo wakati alipotembelea chuo cha Usafirishaji Tanzania (NIT) jijini Dar es Salaam leo Julai 24, 2026.


Na Mwandishi Wetu
SERIKALI imekitaka Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) kuhakikisha kinakamilisha miradi yote ya maendeleo inayoendelea na kuongeza juhudi za kuzalisha wataalamu wenye uwezo wa kufanya kazi ndani na nje ya nchi ili kuunga mkono utekelezaji wa miradi mikubwa ya miundombinu ya usafiri inayotekelezwa nchini.

Rai hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile, Julai 24, wakati alipotembelea chuo hicho kwa niaba ya Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa, kwa lengo la kukagua maendeleo ya miradi na kujionea namna serikali ilivyowekeza katika kuimarisha mafunzo ya sekta ya usafiri.

Kihenzile amesema Serikali inaendelea kutekeleza miradi mikubwa ya usafiri wa anga, barabara, reli na majini, hivyo kuna umuhimu wa kuwa na wataalamu wa kutosha watakaosimamia na kuendesha miradi hiyo.

Amesema ameridhishwa na maendeleo ya ujenzi wa miundombinu ya chuo hicho, ikiwemo majengo yenye thamani ya zaidi ya Sh bilioni 70 yaliyofadhiliwa na Serikali ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa lengo la kuongeza uwezo wa chuo kutoa mafunzo ya kisasa.

"Rai yangu kwa uongozi wa chuo ni kuhakikisha miradi yote inakamilika kwa wakati na muendelee kubuni programu zitakazozalisha wataalamu wa sekta ya anga, majini na ardhini. Hatupaswi kuendelea kutegemea wataalamu kutoka nje wakati tuna vijana wenye uwezo mkubwa," amesema.

Pia amesema miongoni mwa miradi aliyotembelea ni jengo maalumu la mafunzo ya matengenezo ya ndege, jengo la mafunzo kwa wahudumu wa ndege, madarasa ya marubani pamoja na mabweni ya kisasa yenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 1,500.

Aidha, amesema idadi ya wanafunzi chuoni hapo imeongezeka hadi kufikia zaidi ya 19,000, jambo linaloonesha kukua kwa mahitaji ya wataalamu wa sekta ya usafirishaji nchini.

Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi la Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), Prof. Ulingeta Obadia Mbamba, amesema ziara ya Naibu Waziri imewapa hamasa ya kuongeza ubunifu na kuhakikisha chuo kinaendelea kuwa kinara katika kuzalisha wataalamu wa sekta ya usafiri.

Amesema Serikali imewekeza kwa kiwango kikubwa katika sekta ya usafiri, hivyo chuo kina wajibu wa kuhakikisha kinaandaa wataalamu watakaoweza kuendesha maendeleo hayo na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.

"Naibu Waziri ametusisitiza tusiridhike na mafanikio tuliyofikia, bali tuendelee kuboresha mazingira ya kujifunzia na kuongeza ubora wa mafunzo ili wataalamu wanaohitimu hapa waweze kushindana katika soko la ajira la kimataifa," amesema Mbamba.

Aidha, amesema chuo kitaendelea kutekeleza maelekezo hayo ili kuendana na kasi ya maendeleo ya sekta ya usafiri, ambayo imeendelea kuwa mhimili muhimu wa kukuza uchumi na utoaji wa huduma nchini.





Matukio mbalimbali katika 
picha za pamoja.

WANANCHI wa Jimbo la Monduli wamempokea kwa shangwe Mlezi wao wa Mkoa wa Arusha ambaye pia ni Waziri wa Kilimo, Mhe. Daniel Chongolo (Mb) na kutuma salamu kuwa wako bega kwa bega na Serikalini katika kuleta maendeleo nchini.

Salamu hizo zimetolewa tarehe 23 Julai 2026 wakati wa mkutano wa hadhara wa Mhe. Waziri Chongolo na maelfu ya wananchi waliojikusanya katika eneo la Soko la Losirwa, Kata ya Esilalei, Wilaya ya Monduli.

“Hongereni kwa kujibiidiisha kwa kazi. Nimepokea kilio chenu cha kujengewa soko la kisasa la Losirwa, niwahakikishie Wizara itafanyia kazi hilo; sambamba na kukamilisha ukarabati wa skimu ya umwagiliaji ya Mto wa Mbu kwa gharama ya shilingi bilioni 17 chini ya Tume ya Taifa ya Umwagiliaji ili kutatua matatizo ya kilimo cha umwagiliaji katika Kata za Wilaya ya Monduli,” amesema Mhe. Chongolo.

Akizungumza kwa niaba yao, Mbunge wa Jimbo la Monduli Mhe. Joseph İsack Copiriano amesema kuwa wananchi wa Monduli wanaipongeza Serikali kwa kusogeza huduma za kijamii na kupeleka miradi ya maendeleo ikiwemo elimu, afya na kilimo.

“Kilio chao ni mbolea ipatikane, wanahitaji maji na ujenzi wa barabara, ikiwa ni pamoja na kupata elimu zaidi kuhusu kilimo cha malisho ya mifugo,” ameeleza Mhe. Copiriano.

Akijibu hoja za wananchi, Mhe. Chongolo ameahidi kuwa zitafanyiwa kazi na Wizara ya Kilimo na Taasisi zake, huku akisisitiza kwa wananchi umuhimu wa kulinda miundombinu na vyanzo vya maji kwa kuwa mabwawa madogo yanaweza kujengwa maeneo hayo kwa ajili ya shughuli za kilimo na kunywesha mifugo.

Katika nyakati tofauti, Waziri Chongolo pia ametembelea Shule ya Sekondari ya Manyara yenye wanafunzi zaidi 1,800 na kuzindua bweni la wanafunzi wavulana.











Na Mwandishi Wetu
JESHI la Polisi Mkoa wa Shinyanga limetekeleza matendo ya huruma kwa kutembelea na kuwafariji wagonjwa wanaopatiwa matibabu katika Kituo cha Afya Kambarage, kilichopo Manispaa ya Shinyanga, huku likitoa ujumbe wa matumaini, maadili na usalama kwa wananchi.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mkuu wa Polisi Jamii Mkoa wa Shinyanga, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Fraterine Tesha amesema Jeshi la Polisi linatambua kuwa wagonjwa ni sehemu ya jamii inayolihudumia na kulilinda, hivyo limeona ni muhimu kufika kituoni hapo kuwapa pole na kuwatia moyo.

ACP Tesha, amewaasa wagonjwa kuwa na uvumilivu wakati wa matibabu, akisisitiza kuwa jamii inaendelea kuwaombea ili wapone na kurejea katika shughuli zao za kila siku za kushiriki ujenzi wa Taifa.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani Wilaya ya Shinyanga, Mrakibu Msaidizi wa Polisi (ASP) Zainabu Mangara, amewapongeza wanawake waliojifungua katika kituo hicho cha afya na kuwakumbusha umuhimu wa kulea watoto wao katika misingi ya maadili mema.

ASP Mangara, ametoa elimu ya usalama barabarani kwa wazazi hao, akiwakumbusha kutowaruhusu watoto wao kupandishwa kwenye pikipiki zaidi ya mtoto mmoja kwa wakati mmoja, akieleza kuwa kitendo hicho kinaongeza hatari ya ajali na kuhatarisha maisha ya watoto pamoja na watumiaji wengine wa barabara.

Akizungumza kwa niaba ya uongozi wa Kituo hicho, Mganga Mfawidhi Dkt. Ernest Kurwa amelishukuru Jeshi la Polisi kwa kutenga muda wa kutembelea na kuwafariji wagonjwa.

Dkt. Kurwa amesema ziara za aina hiyo huwapa wagonjwa faraja na matumaini, huku akitoa wito kwa jamii kujenga utamaduni wa kutembelea wagonjwa hospitalini ili kuwapa moyo na kuwafanya wajione kuwa hawapo peke yao katika kipindi cha changamoto za kiafya.

Top News