Wananchi wa Kata ya Chang'ombe na Totowe, Wilaya Songwe Mkoa wa Songwe, wametakiwa kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi katika  kupambana na uhalifu, hususan vitendo vya ukatili dhidi ya watoto, kwa kutoa taarifa za uhalifu na wahalifu ili hatua za kisheria zichukuliwe kwa wakati.

Kauli hiyo ilitolewa na Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Mh. Jabiri Makame, Julai 22, 2026, wakati wa ziara kampeni  inayoitwa kwa  jina la Serikali Nyumbani Kwako, ambapo alisisitiza kuwa vitendo vya ukatili dhidi ya watoto havikubaliki, huku akieleza kuwa ni wajibu wa kila mwananchi kuwalinda, kuwatunza na kuwalea watoto kwa upendo kwa kuwa ndiyo msingi wa taifa la kesho.

Akizungumza katika ziara hiyo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Songwe, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Augustino Senga, aliwataka wananchi kupiga vita matukio ya ubakaji na ulawiti katika  maeneo yote, hivyo kila mwananchi ana wajibu wa kulinda watoto wa kike na wa kiume pamoja na kuheshimu haki na usalama wa watu wote katika jamii.

Aidha Kamanda Senga aliwasisitiza wananchi  kupambana dhidi ya makosa hayo maana yanahitaji ushirikiano wa wananchi  na Jeshi la Polisi katika kutoa taarifa za uhalifu kwa kuyazuia matukio hayo kabisa katika jamii.

Pia Kamanda Senga aliwataka wananchi kuachana na matumizi mabaya ya fedha kwa mambo yasiyo na tija na badala yake kuelekeza rasilimali katika kuboresha maisha ya familia, malezi ya watoto na shughuli za maendeleo. 

Mwisho, Kamanda Senga alimalizia kwa kutoa wito kwa wananchi wote kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kuzuia na kupambana na uhalifu, akieleza kuwa ushirikiano huo utasaidia kukomesha ubakaji, ulawiti, ulevi wa kupindukia na vitendo vingine vya kihalifu ili kujenga jamii salama, yenye amani na inayowalinda watoto. 









 


Na. Mwandishi wetu Jeshi la Polisi

NDOTO za vijana wanaoishi katika mazingira magumu mkoani Arusha zimeanza kupata mwanga baada ya Jeshi la Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani mkoani humo, kuzindua mpango wa kuwabaini na kuwapa mafunzo ya udereva bila malipo kwa kushrikiana na vyuo vya udereva, hatua inayolenga kuwajengea ujuzi na kuwainua kiuchumi.

Akizungumza mara baada ya kufungua mafunzo hayo leo, Mkuu wa Kikosi cha Usalama barabarani mkoani humo, ACP Zauda Mohamed amesema mpango huo ni sehemu ya mkakati wa kuwawezesha vijana, ili kuwaondoa kwenye mazingira magumu yanayoweza kuwashawishi kujihusisha na vitendo vya kihalifu kwa kuwapatia ujuzi utakaowajengea uwezo wa kujitegemea.

ACP Zauda amebainisha kuwa, vijana hao waliwachukua kutoka sehemu mbalimbali ikiwemo vituo vya kulelea watoto wenye changamoto za malezi, maeneo ya kuegesha na kuosha magari, wanaobeba mizigo sokoni pamoja na wapiga debe katika vituo vya mabasi.

Aidha, amefafanua kuwa pamoja na kugharamia mafunzo hayo, Jeshi hilo pia litahakikisha linawasimamia vijana hao katika hatua zote za kupata leseni za udereva ili kuongeza fursa zao za kujiajiri au kuajiriwa mara baada ya kuhitimu mafunzo.

Mkuu huyo wa usalama barabarani amemaliza kwa kusema kuwa, anaamini kuwa baada ya vijana hao kuhitimu na kupata leseni zao za udereva, itakuwa ni chachu ya mabadiliko kwao kiuchumi, kuwaondoa katika makundi hatarishi lakini poa kuwaepusha na uhalifu.

Naye Bw. Godfrey Laizer, mnufaika wa mafunzo hayo anayejishughulisha na kubeba mizigo amesema mafunzo hayo yamempa matumaini mapya, akieleza kuwa yatamwezesha kupata leseni ya udereva na kufungua fursa za ajira pamoja na kuboresha maisha yake.

Kijana kutoka kituo cha kulelea watoto yatima cha Kindness Children Care, Bw. Steven Daniel amelishukuru Jeshi la Polisi kwa fursa hiyo, akisema watajituma katika mafunzo ili kutimiza ndoto zao za badaye.

Kwa upande wake Bi. Emmy Frank anayejishughulisha na kuosha magari amesema mafunzo hayo yatamjengea ujuzi na kumpa nafasi ya kupata ajira zenye kipato bora. Ameahidi kuitumia vyema fursa hiyo na kuzingatia mafunzo yote atakayopatiwa.


SERIKALI imeagiza Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) kuhakikisha inasimamja usambazaji wa mbolea kwa wakulima nchini wakiwemo wakulima wa kijiji cha Mang’ola, Wilaya ya Karatu Mkoani Arusha.

Amesema Waziri wa Kilimo, Mhe. Daniel Chongolo (Mb) akiwa katika ziara ya kikazi mkoani humo tarehe 22 Julai 2026 ili kukagua miradi ya maendeleo.

“Niwapomgeze wananchi wa Mang’oa kwa kujishughulisha na kilimo cha vitunguu na mazao memgime. Nimeielekeza TFRA na Kampuni ya Mbolea Tanzania (TFC) kuhakikisha mbolea inayosambazwa nchini inawafikia,” amesema Waziri Chongolo.

Aidha, Mkurugenzi Mkuu wa TFC, Bw. Samwel Mshote amesema kuwa tani elfu mbili za mbolea ya DAP zinapelekwa ndani ya wiki mbili katika kijiji hicho huku taratibu za kuwa na myrndaji wa TFC kuwepo Mang’oa zitatekelezwa ili wakulima wapatiwe elimu ya matumizi sahihi ya mbolea.

Sambamba na hilo, Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) Joel Lauren amesema kuwa wakulima wataendelea kupatiwa mafunzo ya matumizi sahihi ya mbolea kupitia Kampeni ya Mali Shambani inayoratibiwa na Wizara ya Kilimo kuanzia mwezi Agosti 2026 .

Ameeleza kuwa “matumizi mbadala si kununua mbolea kwa jina badala yake ni kuwa na elimu ya sahihi ya matumizi ya mbolea kwa kuendana na virutubisho, afya ya udongo na mbegu bora.”

Kuhusu biashara holela ya mbolea, Bw. Laurent amesema kuwa hakuna mfanyabiashara atakayeruhusiwa kuuza mbolea kinyume na masharti ya leseni yake na moja ya adhabu ni kufutiwa leseni. Mpango wa ruzuku bado upo kupitia maelekezo ya Serikali ambayo imetoa fedha kuhakikisha mkulima anapata bei himilivu ya mbolea.




















SERIKALI  imewaahidi wakazi wa kijiji cha Endashangwet, Wilayani Karatu katika Mkoa wa Arusha kuwa ujenzi wa soko la vitunguu ukikamilika kwa awamu zote litakuwa soko la kuuza vitunguu masoko ya kimataifa zaidi ya soko la Kenya.

Ametoa ahadi hiyo Waziri wa Kilimo, Mhe. Daniel Chongolo (Mb) akiwa ziarani Arusha kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo na Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2025–2030, tarehe 22 Julai 2026, ambapo ameambatana na Viongozi mbalimbali wa Serikali kutatua kero za wananchi kama mlezi wa Mkoa huo. 

“Nimepokea ombi la Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Arusha (CCM), Mhe. Cecilia Pareso la kupanua ukubwa wa soko hili.  Naielekeza Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA) kuhakikisha inaanza mchakato wa kupanua ujenzi wa soko, huku ikitafuta masoko mengine ya vitunguu nje ya nchi.  Dhamira ya Serikali ni kuona wakulima wa vitunguu katika Wilaya ya Karatu sasa wanakuwa na soko la kuuza vitunguu wanavyozalisha kimataifa kutokana na ubora wake,” amesema Mhe. Daniel Chongolo.

Awamu ya kwanza ya ujenzi wa soko la kijiji cha Endashangwet lenye gharama ya Shilingi Milioni 500 imepangwa kukamilika mwezi Novemba mwaka huu, ambapo Waziri Chongolo amesisitiza ubora wa miundombinu katika ujenzi huo uzingatiwe.  

Wilaya ya Karatu imejikita na shughuli mbalimbali za maendeleo wakiwemo wakulima wanaolima mazao ya vitunguu, ngano, mbaazi, mahindi na maharage







Na Mwandishi Wetu
WIZARA ya Afya, Ofisi ya Waziri Mkuu Tamisemi  imekutana na wataalam mbalimbali wanaotoa huduma za Afya Ngazi za Jamii Wilayani Bukombe Mkoani Geita kwa lengo la kuwajengea uwezo kuhusu utekelezaji wa Mpango Jumuishi wa Wahudumu wa Afya Ngazi Jamii.

Mkuu wa Wilaya ya Bukombe Paskasi Muragili amesema Wahudumu  wa Afya Ngazi ya Jamii ni muhimu sana katika kutoa Elimu ya Afya kwa jamii kwani Wilaya ya Bukombe bado inakabiliwa na changamoto ya malaria,lishe pamoja na  changamoto za Afya ya Mama na Mtoto.

Kiongozi huyo amebainisha hayo leo tarehe 22 Julai, 2026 Wilayani Bukombe Mkoani Geita wakati wa Ufunguzi wa Kikao Kazi hicho kilichowakutanisha kamati tendaji za kata, baadhi ya watoa huduma za afya ngazi ya jamii na Waganga wafaidhi wa Vituo vya Afya.

Bw. Muragili ameangazia umuhimu wa huduma inayotolewa na Muhudumu wa Afya Ngazi ya Jamii kuliko mchakato wa upatikanaji wake akiangazia namna ambavyo serikali ya sasa ilivyowekeza katika kuokoa maisha ya mama na mtoto.

‘’Kama mtoa huduma za Jamii atatoa Elimu ya Afya mapema na mama akaanza mapema huduma za kliniki tutapunguza kwa kabisa vifo vya mama na mtoto, ikiwemo malaria na afua mbalimbali za lishe,’’aliongeza Kiongozi huyo.

Naye Afisa Mpango wa Wahudumu wa Afya Ngazi ya Jamii kutoka Wizara ya Afya Bahati Mwailafu amesema Wahudumu hao wanapatiwa elimu ya utekelezaji wa Mpango huo akiitaja Bukombe kuwa eneo la Mfano kati ya Halmashauri zinazotekeleza Mpango huo kuanza kupima na kutoa dawa kwa wagonjwa wa malaria.

‘’Bukombe ni Halmashauri ya mfano iliyochaguliwa kwenye Halmashauri 184 nchini inayojengewa uwezo wa kupima malaria katika kaya na kutoa dawa’’, aliongeza Bw. Mwailafu.  

Akiwasilisha mada yake kwa wajumbe wa Kikao kazi hicho Afisa Mpango wa Wahudumu wa Afya Ngazi ya Jamii kutoka Wizara ya Afya Bi. Orsolina Tolage amesema Muhudumu wa Ngazi ya Jamii anawajibika kushiriki katika vikao vya Kijiji na kupewa fursa ya kutoa Mawazo kuhusiana na huduma za kiafya zinazotolewa katika Kituo husika.

Muhudumu wa Afya Ngazi ya Jamii kwa mujibu wa Mwongozo anafanya kazi katika yale maeneo ya Jamii ambayo yako katika mazingira ambayo hayana vituo vya Afya na taarifa zao kutumiwa na wataalam wa Afya kufanyia kazi changamoto zilizoibuliwa na muhudumu husika.

 

Wapanda Mlima wa kampeni ya GGM HIV Kili Challenge baada ya kuwasili katika uwanja wa Kimataifa wa KIA kwa ajili ya kuanza zoezi la kupanda mlima Kilimanjaro siku  ya Ijumaa




Na Mwandishi Wetu
Shamrashamra na hamasa zimetawala katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) baada ya washiriki wa kampeni ya GGM HIV Kili Challenge kuwasili tayari kwa kuanza safari ya kupanda Mlima Kilimanjaro na kuuzunguka kwa baiskeli, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuchangisha fedha na kuhamasisha mapambano dhidi ya Virusi vya Ukimwi (VVU) nchini.

Safari hiyo rasmi inaanza siku ya Ijumaa, ambapo jumla ya watu 38 watapanda Mlima Kilimanjaro kwa miguu, huku washiriki wengine 10 wakitarajiwa kuuzunguka mlima huo kwa kutumia baiskeli katika kipindi cha siku saba.

Lengo ni kuhamasisha jamii, taasisi na kampuni mbalimbali kuunga mkono kampeni hiyo kupitia michango itakayosaidia utekelezaji wa afua mbalimbali za kupambana na VVU na UKIMWI.

Wakizungumza mara baada ya kuwasili kaika uwanja wa KIA, washiriki hao kutoka mkoani Geita walieleza furaha yao kuwa sehemu ya kampeni hiyo na kuahidi kufanya kila jitihada kuhakikisha wanafika kilele cha Mlima Kilimanjaro.

Mmpja wa washiriki hao ambaye tayari amewahi kushiriki mara mbili zilizopita, Bi. Chitegetse Rushatsi alisema ana imani kubwa ya kufanikiwa kufika kileleni tena safari hii .

"Tumepokelewa kwa furaha kubwa na tuna matumaini makubwa ya kufika kileleni. Hii ni mara yangu ya tatu kushiriki, na mara zote nimefanikiwa kufika kileleni. Najivunia kuwa sehemu ya historia hii," alisema.

Kwa upande wake, Bi. Martha Daniel, ambaye anashiriki kwa mara ya kwanza, alisema kuwa hapo awali alikuwa na hofu, lakini alihamasika baada ya kufahamu umuhimu wa kampeni hiyo.

"Nilipopata taarifa kwamba nimechaguliwa kushiriki nilikuwa na hofu, lakini baada ya kupewa hamasa na kuelezwa umuhimu wa tukio hili niliamua kuwa sehemu ya historia," alisema.

Aliwahimiza wanawake kujitokeza kwa wingi kushiriki katika kampeni hiyo, akisema mbali na kusaidia mapambano dhidi ya VVU, pia inachangia kutangaza na kuhamasisha utalii wa ndani.

Bi. Martha pia aliushukuru mgodi wa Dhahabu wa Geita (Geita Gold Mining Limited -GGML) kwa kuweka mazingira yanayowawezesha wafanyakazi wake kushiriki katika shughuli za kijamii zenye manufaa kwa jamii na taifa kwa ujumla, pamoja na kuipongeza kampuni ya Ahsante Tours kwa kuwa waongozaji wakuu wa safari hiyo.

Katika kuonesha kuwa kampeni hiyo inawahusisha watu wa rika mbalimbali, Marietha Elius, mwanafunzi wa Darasa la Saba mwenye umri wa miaka 13, ni mmoja wa washiriki wa safari hiyo.

Marietha alisema amefurahia kupata nafasi ya kupanda mlima mrefu zaidi barani Afrika huku akichangia jitihada za kuwasaidia watu wanaoishi na VVU.

"Nina furaha mara mbili; kwanza kushiriki kuwasaidia watu wanaohitaji msaada, na pili kupata nafasi ya kuuona na kuupanda Mlima Kilimanjaro ambao wengi wetu tunaujifunza darasani kupitia historia yake," alisema.

Akizungumza kwa niaba ya menejimenti ya GGML, Bw.Gilbert Mworia alisema mwitikio wa wadau katika kampeni ya mwaka huu umeongezeka kwa kiwango kikubwa ikilinganishwa na miaka iliyopita.

Alisema ongezeko hilo linaonesha dhamira ya wadau mbalimbali kuunga mkono lengo la kufanikisha malengo ya Sifuri Tatu ifikapo mwaka 2030, ambayo inalenga kutokomeza maambukizi mapya ya VVU, kuzuia vifo vinavyotokana na UKIMWI na unyanyapaa dhidi ya watu wanaoishi na VVU. Mworia aliongeza kuwa mwaka huu, kama ilivyokuwa katika miaka ya nyuma, kampeni hii itaambatana na huduma za upimaji wa VVU na uchangiaji wa damu salama zitakazotolewa katika maeneo mbalimbali ya wananchi, tofauti na miaka iliyopita ambapo huduma hizo zilitolewa katika malango ya Machame na Mweka pekee wakati wa upandaji wa mlima.

Kampeni ya GGM HIV Kili Challenge inaratibiwa na GGML kwa kushirikiana na Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS) pamoja na wadau mbalimbali. Mbali na kuchangisha fedha kwa ajili ya huduma kwa watu wanaoishi na VVU, kampeni hiyo inalenga kutoa elimu kwa jamii, kupunguza unyanyapaa na kusaidia ujenzi wa miundombinu pamoja na huduma nyingine muhimu katika harakati za kutokomeza UKIMWI nchini.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla, amefungua rasmi Kituo cha Malezi na Makuzi ya Awali ya Mtoto (ECD) cha Mwanakwerekwe kilichofadhiliwa na Stanbic Bank Tanzania, sambamba na uzinduzi wa Mpango wa Zanzibar wa Malezi na Makuzi ya Awali ya Mtoto wa Kisekta (2026–2031).

Ufadhili wa kituo hicho umetokana na awamu ya kwanza ya TZS milioni 350 iliyotolewa na Stanbic Bank Tanzania, ikiwa ni sehemu ya ahadi ya benki hiyo ya TZS milioni 500 kwa mpango wa Serikali wa Adopt an ECD unaoendeshwa na Shirika la Save the Children.

Kituo hicho kitatoa huduma bora za malezi na elimu ya awali kwa watoto wa wafanyabiashara na familia zinazofanya kazi katika Soko la Mwanakwerekwe na maeneo jirani.

“Uwekezaji huu unaakisi dhamira ya Stanbic Bank Tanzania ya kuendeleza malezi na makuzi ya awali ya mtoto kama msingi wa kujenga rasilimali watu, kukuza uchumi shirikishi na kuimarisha ustawi wa muda mrefu wa Zanzibar. Aidha, unaonesha mafanikio yanayowezekana pale Serikali, sekta binafsi na washirika wa maendeleo wanapounganisha nguvu kuelekea dira moja,” amesema Derick Lugemala, Afisa Mkuu wa Fedha, Stanbic Bank.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kituo hicho, Mhe. Hemed aliipongeza Stanbic Bank kwa kuunga mkono ajenda ya serikali ya kuwekeza katika maendeleo ya mtoto katika umri wa awali na kuzitaka benki nyingine pamoja na taasisi za kifedha kuiga mfano huo wa kuchangia maendeleo ya taifa.

"Tunaipongeza Benki ya Stanbic kwa uwekezaji huu wa kimkakati na mchango wake endelevu katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi, si Zanzibar pekee bali Tanzania nzima kwa ujumla. Nazihimiza benki nyingine na taasisi za kifedha kuiga mfano huu mzuri wa kushiriki katika ujenzi wa taifa," alisema kabla ya kukifungua rasmi kituo hicho kilichopewa jina la Kituo cha Malezi ya Watoto cha Dkt. Hussein Ali Mwinyi.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla (katikati), akimwakilisha Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, akikata utepe kuzindua rasmi Kituo cha Malezi ya Watoto cha Dkt. Hussein Ali Mwinyi kilichopo Mwanakwerekwe, Zanzibar. Wanaoshuhudia ni Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe. Anna Athanas Maalim, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais  Ikulu, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mhe. Saada Mkuya Salum, na Afisa Mkuu wa Fedha wa Stanbic Bank Tanzania, Derick Lugemala. Kituo hicho kimefadhiliwa  na Benki ya Stanbic kinacholenga kupanua upatikanaji wa huduma bora za malezi, makuzi na elimu ya awali kwa watoto nchini Zanzibar.







Kikosi cha usalama barabarani Wilaya ya Ileje kimeungana na wasafirishaji wa abiria kwa kutumia bajaji kuwafariji na kuwasaidia wagonjwa waliolazwa katika Wodi ya Wazazi ya Hospitali ya Wilaya ya Ileje pamoja na wanafunzi wa Shule ya Msingi Mpakani waliofiwa na wazazi wao kwa kuwapatia mahitaji mbalimbali, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha ushirikiano kati ya Jeshi la Polisi na jamii kupitia matendo ya huruma kwa jamii. (Bajaji Day)

Tukio hilo limefanyika Julai 22, 2026 na kuongozwa na Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani Wilaya ya Ileje, Mrakibu Msaidizi wa Polisi (ASP) Krisbert Kapondo, likihusisha viongozi na wanachama wa umoja wa wasafirishaji wa abiria kwa kutumia bajaji. 

Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo, ASP Kapondo aliwapongeza wasafirishaji hao kwa moyo wao wa kujitolea na kuwahimiza kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi katika shughuli mbalimbali za maendeleo ya jamii, akieleza kuwa vitendo vya huruma na upendo vinaimarisha mshikamano, amani na ustawi wa wananchi.

Kwa upande wao, viongozi wa wasafirishaji wa bajaji wakiongozwa na Mwenyekiti wa Bajaji Wilaya ya Ileje, Bw. Domenick Kamwela, pamoja na Diwani wa Kata ya Isongole, Mh Obeid Mwambene walieleza kuwa wataendelea kushiriki katika shughuli za kijamii zinazolenga kuwasaidia wenye uhitaji, huku wakitoa wito kwa wadau wengine kuendeleza utamaduni wa kusaidiana ili kujenga jamii yenye mshikamano, upendo na uwajibikaji. 











Top News