Dar es Salaam, Machi 28, 2026 — Viongozi wa dini nchini wameeleza wasiwasi wao kuhusu kuendelea kwa ndoa za utotoni, wakibainisha kuwa changamoto ya uelewa mdogo wa sheria kuhusu umri sahihi wa kuolewa bado ni kubwa, hasa katika maeneo ya vijijini.

Akizungumza katika kikao cha kitaifa cha viongozi wa dini kuhusu mabadiliko ya kisheria ya ndoa kilichofanyika Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Halmashauri Kuu ya BAKWATA, Sheikh Khamisi Mtaka, alisema pamoja na jitihada mbalimbali zinazofanyika kukomesha ndoa za utotoni, bado kuna mkanganyiko mkubwa kati ya sheria za nchi, mafundisho ya dini na mitazamo ya kijamii.

Alisema hali hiyo imekuwa kikwazo kikubwa katika utekelezaji wa juhudi za kupambana na tatizo hilo.

Sheikh Mtaka alifafanua kuwa kwa sasa hakuna sheria mahsusi inayokataza moja kwa moja ndoa za utotoni, isipokuwa Sera ya Elimu ya mwaka 2014 inayozuia wanafunzi kuolewa au kupata ujauzito wakiwa shuleni.

“Endapo kipengele hiki kitaingizwa pia katika mifumo ya kijamii na kidini bila kukinzana, kitasaidia kuhakikisha anayetarajiwa kuolewa anakuwa amekomaa kiakili,” alisema Sheikh Mtaka.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa kuwepo kwa sera na sheria zitakazoainisha bayana umri sahihi wa kuolewa kwa mtoto wa kike, hatua itakayosaidia kulinda haki zao na kuwapa fursa ya kufikia malengo yao maishani.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Songea Catholic Institute of Technical Education, Padri Longino Kamuhabwa, alisema kuwa hata mafundisho ya dini yanasisitiza umuhimu wa ukomavu wa akili kabla ya mtu kuingia katika ndoa.

Akinukuu Biblia (Mwanzo 1:27), Padri Kamuhabwa alisema licha ya agizo la kuzaa na kuongezeka, ndoa inahitaji maandalizi ya kisaikolojia pamoja na uwajibikaji wa hali ya juu.

“Ndoa inajengwa juu ya msingi wa upendo na uwajibikaji, hivyo ni muhimu kuhakikisha mhusika anakuwa na uhuru wa kufanya maamuzi na ukomavu wa kutosha,” alisema.

Naye Afisa kutoka Msichana Initiative alisema tafiti zilizofanywa na taasisi hiyo katika mikoa mbalimbali zimeonesha kuwa ukosefu wa elimu pamoja na mila na desturi bado vinachangia kwa kiasi kikubwa kuendelea kwa ndoa za utotoni vijijini.

Kwa upande wake, Wakili Lucy Gidamis kutoka taasisi hiyo aliongeza kuwa jamii nyingi bado zinaweka mbele maslahi ya kiuchumi badala ya ustawi na haki za mtoto wa kike.

Alisisitiza kuwa tatizo hilo linahitaji juhudi za pamoja kutoka serikalini, viongozi wa dini pamoja na wadau wa maendeleo ili kulipatia ufumbuzi wa kudumu.




Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Bw. Yusuph Juma Mwenda amewataka walipakodi ambao bado hawajafanyiwa makadirio ya kodi kwa nchi nzima kutumia siku mbili zilizosalia kufanya makadirio yao kabla ya kufika kwa muda wa mwisho wa kufanya makadirio ambao ni Machi 31, 2026.

Akizungumza na baadhi ya walipakodi pamoja na waandishi wa habari alipofanya ziara katika kituo cha kodi cha Buguruni kilichopo Vingunguti jijini Dar es Salaam tarehe 29.03.2026 Kamishna Mkuu Mwenda amesema ni vema walipakodi wakautumia muda uliosalia kwenda kufanyiwa makadirio ya kodi.

Amesema TRA imefungua ofisi zake kwa siku za Jumamosi na Jumapili kwa lengo la kuhakikisha kuwa kila mmoja mwenye kutakiwa kufanya makadirio anatekeleza wajibu wake kikamilifu.

Anasema makadirio yanafanywa kwa wale wanaoanza biashara na kwa wale ambao walishaanza biashara huku akiwataka walipakodi kuhakikisha wanafanyiwa makadirio kutokana na aina ya biashara wanayoifanya wanazofanya.

"Moja ya haki ya wanaokadiriwa kulipa kodi ni kwenda kwa maafisa wa TRA ili waweze kukadiriwa, kama wataona kiasi walichokadiriwa ni kidogo wanayo haki ya kuwaeleza maafisa wetu, lakini pia kama wakiona kiasi walichokadiriwa ni kikubwa pia wanayo haki pia ya kuwambiwa maafisa yetu ili wafanyiwe upya makadirio" amesema Mwenda

Kwa Upande wake Meneja wa Kituo Cha Huduma za Kodi Cha Buguruni Mamika Nyika amewataka wafanyabiashara na watoa huduma wote kuhakikisha wanatumia kikamilifu siku tatu zilizobaki ili kujiepusha na adhabu na kusisitiza kuwa milango ya Ofisi hiyo ipo wazi kwa ajili ya kuwahudumia

Naye mmoja wa walipakodi katika kituo hicho Bw. Masoud Kumbakumba mbali na kutoa rai kwa wafanyabiashara wenzie kutumia muda uliobaki kujitokeza kulipa Kodi, amesema tofauti na miaka ya nyuma, hivi sasa TRA imekuwa ikitoa ushirikiano mkubwa kwa wafanyabiashara jambo linalowavutia kujitokeza kulipa Kodi.

Amesema Kipindi cha nyuma ilikuwa ngumu kuwaona wafanyabiashara wakienda kwa hiari katika Ofisi za TRA hali iliyotokana na uwepo wa hofu miongoni mwao, ila kwa sasa hakuna hali kama hiyo jambo linaloongeza wigo wa ulipaji wa Kodi kwa hiari.


Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Imeelezwa kuwa licha ya mvutano wa kisiasa, hususan Mashariki ya Kati unavyoendelea kubadilisha mifumo ya biashara, masoko ya nishati na mwelekeo wa uwekezaji wa mitaji, Tanzania bado itaendelea kuwa eneo lenye kuaminika kwa uwekezaji wa muda mrefu — iwapo itachukua hatua mbalimbali ili isiathirike na machafuko hayo kiuchumi.

Hayo yameelezwa katika mjadala wa hivi karibuni ulioandaliwa na ALN Tanzania (A&K Tanzania) kwa kushirikiana na Bankable, ambapo viongozi waandamizi kutoka sekta za benki, viwanda na nishati walijadili namna mabadiliko ya kimataifa yanavyoathiri maamuzi ya uwekezaji duniani na maana yake kwa nafasi ya ushindani ya Tanzania.

Ukiwa na kauli mbiu “ Dunia inayobadilika- Faida ya ushindani wa Tanzania ” , wadau walibainisha kuwa Tanzania bado ni eneo linalovutia kwa uwekezaji, licha ya mazingira ya uwekezaji kuwa magumu hivi sasa katika nchi nyingi. Upatikanaji wa fedha umepungua, na wawekezaji sasa wanazingatia zaidi usalama wa mitaji yao katika nchi wanazowekeza.

“Mitaji bado ipo, lakini vigezo vimebadilika,” alisema Bw. Ed Williams, Mkurugenzi wa ALN Tanzania. “Sasa swali sio tu kama fursa za biashara bado zipo, bali kama zinaweza kutekelezwa kwa wakati kutokana na hali ilivyo hivi sasa.”

Mjadala huo ulifanyika huku misukosuko ya kimataifa katika Mashariki ya Kati ikiendelea, ambayo imesababisha ongezeko la bei ya mafuta kwa takriban asilimia 20 na kuvuruga njia muhimu za usafirishaji. Kwa Afrika Mashariki, hali hii imesababisha kuongezeka kwa gharama za usafirishaji na kutokuwa na uhakika katika minyororo ya ugavi.

Hata hivyo, wazungumzaji walisisitiza kuwa misukosuko hii pia inachochea mabadiliko mapana ya kimataifa — ambayo yanaweza kuipa Tanzania fursa.

Minyororo ya ugavi inapungua, uwekezaji wa mitaji unatishiwa na hali iliyopo ambapo wawekezaji wanatafuta masoko tulivu yenye nafasi nzuri ya kikanda.

Uwepo wa hali ya utulivu katika Bahari ya Hindi hapa nchini, miundombinu inayoboreshwa, rasilimali asilia na utulivu wa kisiasa vinaipa nafasi nzuri Tanzania kunufaika na mabadiliko ya biashara na uwekezaji.

Bw. Manzi Rwegasira, Mtendaji Mkuu wa Stanbic Bank Tanzania, alibainisha kuwa ingawa hali ya sasa inaathiri moja kwa moja bei za bidhaa, pia inaonesha umuhimu wa uwepo wa masoko thabiti na imara.

Vilevile, Mohamed Mohamed, Mtendaji Mkuu wa kampuni ya kimataifa ya Tanzania ya kuhifadhi mafuta (TIPER), alieleza kuwa miundombinu ya usafirishaji — ikiwemo bandari na uwezo wa kuhifadhi bidhaa za mafuta — inakuwa kigezo muhimu cha ushindani kadiri minyororo ya ugavi ya kimataifa inavyobadilika.

Kwa upande wake, Bw. Vineet Verma, Meneja Mkuu wa Kioo Limited, aliongeza kuwa wazalishaji wanazidi kutathmini maeneo ya kupanua uzalishaji kwa kuzingatia si gharama pekee, bali pia uhakika wa nishati, usafirishaji na upatikanaji wa masoko ya kikanda — maeneo ambayo Tanzania inaendelea kufanya vizuri.

Wazungumzaji walikubaliana kuwa fursa ya Tanzania haitokani tu na rasilimali zake, bali pia na jinsi inavyoweza kuzitumia kwa ufanisi katika mazingira magumu ya kimataifa.

“Misukosuko ya kimataifa imefungua dirisha la fursa kwa masoko kama Tanzania,” alisema Bi. Shemane Amin, Mshirika wa ALN Tanzania. “Tuna msingi mzuri — eneo, rasilimali na utulivu — lakini kitakachotutofautisha ni uthabiti wa utekelezaji na namna tunavyojiweka kama mshirika wa kuaminika wa muda mrefu kwa wawekezaji na mitaji.”

Akiwasilisha andiko lake, Bw. Atiq Anjarwalla, Mshirika Mwandamizi wa ALN (Falme za Kiarabu), alihimiza Tanzania na nchi nyingine za Afrika Mashariki kutumia kwa mkakati rasilimali zao za asili ili kuimarisha uchumi na kujilinda dhidi ya athari za migogoro ya Mashariki ya Kati.

Alisisitiza kuwa hali ya sasa ya kimataifa inaleta changamoto pamoja na fursa, na kuzitaka serikali kuchukua hatua za haraka kuimarisha masoko yao na kuongeza ustahimilivu wa kiuchumi.

“Mfumuko wa bei utaongezeka, na gharama ya maisha itapanda kwa kiasi kikubwa,” alionya. “Bila hatua madhubuti, tunaweza hata kushuhudia kupungua kwa shughuli za usafiri kutokana na kupanda kwa gharama za mafuta.”

“Uvunjifu wa minyororo ya ugavi utavuruga shughuli za biashara na unaweza kuathiri ukusanyaji wa mapato ya kodi, hivyo kudhoofisha uthabiti wa uchumi,” aliongeza.

Akihitimisha, Bw. Chris Green, Mkurugenzi wa ALN Tanzania, alisema kuwa matukio ya hivi karibuni Mashariki ya Kati yameongeza hali ya kutotabirika katika masoko ya kimataifa, na kutoa wito kwa Tanzania kuchukua hatua madhubuti kulinda nafasi yake ya kikanda katika biashara.

Mjadala huo ulisisitiza kuwa ina nafasi nzuri sana ya kuvutia wawekezaji kuokana na muundo wake wa kijiografia kwa kuzungukwa na nchi kadhaa zisizo na bahari, , mazingira wezeshi ya uwekezaji na amani iliyopo.



Na Mwandishi Wetu
SERIKALI inaendelea kujipanga kutunga sheria jumuishi zitakazoshirikisha sekta binafsi kwa lengo la kuimarisha uwezo wa wanawake katika uzalishaji na utengenezaji wa bidhaa zenye ubora na ushindani katika soko la kimataifa.

Akizungumza Machi 28, 2026 jijini Dar es Salaam, Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, amesema hatua hiyo inalenga kuwapa wanawake mazingira bora ya uzalishaji na biashara ili waweze kushindana katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuweka mikakati mbalimbali ya kujenga uchumi jumuishi unaowashirikisha wanawake na vijana kikamilifu katika shughuli za maendeleo.

Kapinga alisema miongoni mwa hatua zilizochukuliwa ni pamoja na kutenga asilimia 30 ya zabuni za manunuzi ya umma kwa makundi maalum, yakiwemo wanawake, vijana na watu wenye mahitaji maalum, hatua inayosaidia kukuza biashara na kuongeza kipato kwa makundi hayo.

Alitoa kauli hiyo katika maadhimisho ya miaka 20 ya Chemba ya Wanawake Wafanyabiashara Tanzania (TWCC) pamoja na msimu wa sita wa utoaji wa tuzo za Viwanda na Biashara kwa wanawake wajasiriamali yaliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Aidha, alisema Serikali inaendelea kuwaongezea wanawake uwezo wa kupata elimu ya teknolojia bunifu ili waweze kuzalisha bidhaa zenye ubora na kukidhi viwango vya soko la kimataifa.

Kwa upande wake, Rais wa TWCC, Mercy Sila, alimpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa juhudi za kuboresha mazingira ya biashara nchini, akisema maboresho katika upatikanaji wa mitaji kupitia madirisha ya wanawake katika benki na mifuko ya uwezeshaji yamepunguza changamoto za upatikanaji wa fedha kwa wanawake wafanyabiashara.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa TWCC, Mwajuma Hamza, amesema chemba hiyo inaendelea kufanya kazi kwa karibu na wadau mbalimbali ili kuwawezesha wanawake kupata mafunzo ya ujasiriamali, uzalishaji na masoko ya kimataifa.

Alisema kupitia juhudi hizo, wanawake wengi wameanza kupanua biashara zao na kupata fursa ya kupeleka bidhaa zao katika masoko ya nje ya nchi, jambo linalochangia kukuza uchumi wa taifa.











‎Mradi wa Uendelezaji Jiji la Dar es Salaam Awamu ya Pili (DMDP II) unatekeleza ujenzi wa barabara zenye urefu wa Kilomita 51.2 kwa kiwango cha lami na zege katika Kata zaidi ya nane (8) na mitaa isiyopungua 20 katika halmashauri ya Manispaa ya Temeke.‎

‎Hayo yamebainishwa na Meneja wa TARURA wilaya ya Temeke, Mhandisi Paul Mhere ambapo ameeleza kuwa wameingia mikataba ya ujenzi wa barabara kwa gharama ya shilingi Bilioni 97.176.

‎"TARURA wilaya ya Temeke tuna mtandao wa barabara Kilomita 648.45, tuna majimbo matatu (3) ambayo ni Temeke, Chamazi na Mbagala na kote miradi inaendelea utekelezaji wake upo zaidi ya asilimia 75 isipokuwa Mbagala na Yombo mikataba ilisainiwa mwezi wa Aprili 2025 utekelezaji wake upo asilimia 32", amesema.

‎Ameongeza kuwa zaidi ya Kilomita 166 za barabara wilayani humo ni lami na zege, barabara za zege zinahimili uzito wa aina yoyote na zinadumu muda mrefu huku zikipunguza matengenezo ya mara kwa mara na kuondolea gharama serikali.

‎‎"Wilaya yetu ina bandari kavu na pia tuna bandari ambayo inahudumia nchi za Afrika Mashariki na Kati, hivyo malori yanayopita katika barabara zetu ni mengi, barabara hizi za zege zitadumu kwa muda mrefu na wananchi wameanza kufurahia maboresho ya miundombinu hii", amesema.

‎Naye, Diwani wa Kata ya Chang'ombe Mhe. Caroline Henrich amesema wamepata barabara sita (6) ambazo ni Igombe-Yemen, Songambele, Majimaji, Basra, Diwani na Mwakalinga ambapo hapo awali kipindi cha mvua maji yalijaa kwenye makazi ya watu na kusababisha kero lakini kukamilika kwa ujenzi wa mitaro sasa maji hayatuami na kero imeondoka pia thamani ya nyumba imepanda.

‎"Namshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mradi huu, awali barabara zilikuwa korofi Kata yetu ni mtambuka barabara kubwa ya VETA na ile inayoelekea Uwanja wa Taifa zikiwa zina foleni hakuna njia nyingine ya kupita zaidi ya barabara zetu, lakini sasa barabara zimejengwa imara kwa kiwango cha zege wageni wengi wanakuja kwa ajili ya biashara", amesema.

‎Kwa upande wake, Mwenyekiti wa mtaa wa Bora, Bw. Pius Kapungu ameeleza kuwa awali kulikuwa na mashimo na kipindi cha mvua maji yalikuwa yanaingia mpaka kwenye makazi ya watu lakini sasa wanashukuru mitaro iliyowekwa imesaidia hakuna maji na taa zikiwekwa kutakuwa salama mitaa itapendeza na ulinzi utaimarika.

‎Aidha, Bi. Saada Salim mkazi wa mtaa wa Majimaji ameipongeza serikali kwa ujenzi wa barabara na mifereji kwani kipindi cha mvua watu walishindwa kupata wateja wa kupangisha lakini sasa wanapata wateja wengi uchumi unakua, mazingira yamekuwa mazuri, maduka yamekuwa mengi na magari yanafika.

‎‎Naye, Bw. Jimmy Mwakipesile mkazi wa Chang'ombe maduka mawili amesema barabara imewarahisishia kusafirisha abiria kwa usalama tofauti na awali walikuwa wanadondoka kwenye maji na matope, pia sasa abiria wameongezeka kwa siku walikuwa wanapata shilingi 15,000 hadi 20,000 lakini sasa wanaweza kupata hadi shilingi 40,000 mpaka 50,000 kwa siku.







Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, ametoa ufafanuzi rasmi kuhusu hatma ya eneo la Coco Beach, akisisitiza kuwa halitauzwa kwa mwekezaji yeyote bali maboresho yatafanyika kwa manufaa ya wananchi waliopo katika eneo hilo.

Amesema hayo leo, Machi 29, 2026, alipotembelea eneo la Coco Beach jijini Dar es Salaam, ambapo alizungumza na wajasiriamali wadogo wanaofanya shughuli zao katika eneo hilo na kusikiliza kero zao mbalimbali.

“Coco Beach haiuzwi. La kwanza niwaondolee hofu—hapauzwi, wala hakuna mwekezaji mwingine zaidi yenu nyinyi wenyewe. Hakuna atakayekuja kutoa maelekezo zaidi ya yale yaliyotolewa na Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan. Hapa hapauzwi,” amesisitiza.

Aidha, Dkt. Mwigulu amesema Serikali itaendelea kutekeleza maelekezo ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa lengo la kuhakikisha Watanzania wananufaika na maboresho yanayofanyika katika eneo hilo.

“Sisi wasaidizi wa Mheshimiwa Rais tutaendelea kuhakikisha Watanzania wanapata lile tabasamu la Mama ambalo amewaahidi,” amesema.

Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu amewataka watendaji wa Manispaa ya Kinondoni, akiwemo Mkuu wa Wilaya, Mkurugenzi wa Halmashauri, Afisa Biashara pamoja na watendaji wengine, kubadili mtindo wa utendaji kazi kwa kuwafuata wananchi moja kwa moja badala ya kuwasubiri ofisini.

“Ninatoa agizo kwa Mkuu wa Wilaya, Mkurugenzi, Afisa Biashara pamoja na watendaji wengine—msikae ofisini tu. Tokeni mkazungumze na wananchi hawa moja kwa moja pale wanapokuwa na masuala yanayowahusu,” amesisitiza.

Kadhalika, Dkt. Mwigulu amewahimiza wajasiriamali wa eneo la Coco Beach kuunga mkono juhudi za Serikali katika maboresho yanayoendelea kufanyika, huku akisisitiza kuwa fursa zitakazotokana na maboresho hayo zitawanufaisha wao wenyewe.






Machi 28, 2026 Na Mwandishi Wetu, Singida

Kampasi ya Singida ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) imekabidhi msaada kwa watoto wenye mahitaji maalum wanaolelewa katika Kituo cha Malaika wa Matumaini kilichopo Ititi, mkoani Singida, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 25 tangu kuanzishwa kwa chuo hicho.

Zoezi hilo limeongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mhe. Godwin Gondwe, akishirikiana na Mkurugenzi wa Kampasi ya Singida, Dkt. Emmanuel Tandika, pamoja na watumishi wa chuo hicho. Msaada huo umewajumuisha vyakula mbalimbali kama mchele, sukari, unga wa sembe na vifaa vya usafi, na umetolewa sambamba na zoezi la kufanya usafi katika mazingira ya kituo hicho.

Mhe. Gondwe, aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Singida, ametoa pongezi kwa Kampasi ya Singida kwa kuonyesha moyo wa kujitolea na kuguswa na jamii, akisema kitendo hicho kimekuwa mfano wa kuigwa na taasisi nyingine katika mkoa huo.

“Kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa, tunapongeza kazi iliyofanywa na Chuo cha Utumishi wa Umma. Utoaji huu wa msaada umeonyesha upendo wa kweli kwa watoto hawa na umeunga mkono juhudi za serikali katika kuwajali makundi maalum,” amesema Mhe. Gondwe.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Kampasi ya Singida, Dkt. Emmanuel Tandika, amesema msaada huo umetolewa kama sehemu ya mchango wa chuo kwa jamii inayolizunguka.

“Tunaposherehekea miaka 25 ya kutoa huduma kwa umma, tumeona ni vyema kuonyesha upendo na mshikamano kwa watoto hawa wenye mahitaji maalum wajue kuwa hawako peke yao, jamii ipo pamoja nao na inawapenda.” Amesema Dkt. Tandika

Aidha, ameeleza kuwa msaada huo umetolewa pia ili kuwapa motisha masista na walezi wanaohudumia watoto hao licha ya changamoto wanazopitia kila siku.

Mlezi wa kituo hicho, Sista Rosalia Nicodemus, kwa niaba ya Mkuu wa Shirika, ameshukuru uongozi wa chuo na serikali ya mkoa kwa msaada huo, akisema umeleta faraja na matumaini kwa watoto wanaolelewa kituoni hapo.

“Kupokelewa kwa wageni kama hawa kumewatia moyo sana watoto wetu,” amesema. “Kwa kweli wamejisikia kupendwa na kuthaminiwa, jambo ambalo limewasaidia kupata nguvu mpya ya kuendelea.”

Sista Rosalia pia ametoa shukrani kwa wadau mbalimbali waliotoa misaada mingine, akiwahamasisha taasisi na watu binafsi kuendelea kushirikiana na kituo hicho kwa kutoa misaada na upendo.

Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kimeendelea kufanya shughuli mbalimbali za kijamii katika kampasi zake za Dar es Salaam, Tabora, Tanga, Singida, Mtwara na Mbeya, kuelekea kilele cha maadhimisho ya miaka 25 kitakaofanyika mwezi Juni 2026.






















Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo amefanya mazungumzo na Balozi wa Italia nchini Tanzania, Mheshimiwa Giuseppe Sean Coppola, aliyemtembelea Ikulu, jijini Dar es Salaam.

Balozi huyo aliambatana na ujumbe kutoka Danieli Group, kampuni inayoongoza duniani katika teknolojia na uhandisi wa uzalishaji wa chuma, ambao wameonesha nia ya kuchunguza uwezekano wa kuwekeza katika sekta ya chuma nchini Tanzania.

Katika mazungumzo hayo, ujumbe huo uliwasilisha nia ya kuanzisha mradi wa ujenzi wa kiwanda cha kisasa na kikubwa cha chuma mkoani Mtwara, kwa kushirikiana na mwekezaji mzawa.

Ushirikiano huu unatokana na majadiliano ya awali yaliyofanyika wakati wa Jukwaa la Biashara na Uwekezaji kati ya Tanzania na Italia, pamoja na mashauriano ya kitaalamu yaliyofuata na taasisi za Tanzania, ikiwemo Mamlaka ya Maeneo Maalum ya Uwekezaji Tanzania (TISEZA) na wizara husika.

Mradi unaopendekezwa, ambao bado uko katika hatua ya awali ya uchambuzi,
unakadiriwa kugharimu takribani Euro bilioni 1.5 (sawa na takribani Shilingi trilioni 4.2 za Kitanzania), na unatarajiwa kutekelezwa kwa awamu kulingana na tathmini zaidi na taratibu za uwekezaji.

Akizungumza katika kikao hicho, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan alikaribisha nia hiyo na kusisitiza dhamira ya Tanzania kuendeleza uwekezaji wa kimkakati unaoendana na vipaumbele vya taifa.

“Tanzania inaendelea kujijenga kama kituo shindani na cha kuaminika kwa uwekezaji,ikitegemea rasilimali zake asilia, nafasi yake ya kimkakati, pamoja na mageuzi yanayoendelea kuboresha mazingira ya biashara,” alisema.

1/2Aliongeza kuwa, “Tunakaribisha ushirikiano unaoongeza thamani ya rasilimali zetu,unaozalisha ajira kwa wananchi wetu, na kuchangia dira yetu ya muda mrefu ya kujenga uchumi wa viwanda.”

Kwa upande wake, Balozi wa Italia alieleza kuwa ushirikiano huo unaakisi kuimarika kwa mahusiano ya kiuchumi kati ya Tanzania na Italia chini ya mifumo mipana ya ushirikiano wa maendeleo.

“Nia iliyooneshwa na Danieli Group ni sehemu ya juhudi pana za kuimarisha ushirikiano kati ya nchi zetu mbili, ikiwemo kupitia Mpango wa Mattei kwa Afrika,” alisema.

Aliongeza kuwa, “Mpango huu unalenga kukuza uwekezaji endelevu na wenye manufaa,kwa pande zote, na Tanzania inaonekana kuwa mshirika muhimu katika muktadha huu.

Kwa sasa, tupo katika hatua ya kuangalia uwezekano na tunatarajia kuendelea
kushirikiana kwa karibu na Serikali ya Tanzania kadri majadiliano yatakavyoendelea.”

Naye Mtendaji Mkuu wa Danieli Group, Bw. Giacomo Mareschi Danieli, alieleza sababu za kimkakati zilizoifanya kampuni hiyo kuvutiwa na Tanzania.

“Tunaona fursa kubwa nchini Tanzania, si tu kutokana na uwepo wa rasilimali kama gesi na madini ya chuma, bali pia kutokana na ukuaji wa soko na nafasi yake ya kimkakati katika ukanda huu,” alisema.

“Mtazamo wetu unalenga ushirikiano wa muda mrefu - kuleta teknolojia ya kisasa
inayozingatia mazingira, huku tukishirikiana na wadau wa ndani kukuza ujuzi na
kujenga uwezo endelevu wa viwanda. Hii ni hatua ya awali, na tumejipanga kuendelea na majadiliano ya kitaalamu ili kutathmini uwezekano wa mradi huu,” aliongeza.

Iwapo utatekelezwa, uwekezaji huu unaweza kuchangia kwa kiasi kikubwa katika ajenda ya Tanzania ya kujenga uchumi wa viwanda chini ya Dira ya Taifa ya 2050, kwa kuimarisha uzalishaji wa ndani wa chuma, kupunguza uagizaji kutoka nje, kuongeza thamani ya rasilimali za ndani, na kutengeneza ajira kwa vijana.

Aidha, unaweza kuimarisha nafasi ya Tanzania kama kitovu cha uzalishaji wa chuma
katika ukanda huu, hususan kwa nchi jirani zisizo na bandari, pamoja na kusaidia
maendeleo ya miundombinu na usafirishaji katika ukanda wa Mtwara.

Mheshimiwa Rais Samia alimhakikishia Mheshimiwa Balozi na ujumbe wake kuwa
Serikali itaendelea kuwa wazi kwa wawekezaji wenye sifa, wanaoleta si mtaji pekee bali pia teknolojia, ujuzi na dhamira ya muda mrefu katika maendeleo ya Tanzania.

Kikao hicho kimeonesha kuendelea kuimarika kwa mvuto wa Tanzania kama kituo cha uwekezaji, pamoja na dhamira ya pamoja ya pande zote mbili kuendele.






Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Balozi wa Italia nchini Tanzania Mheshimiwa Giuseppe Sean Coppola, na ujumbe kutoka DANIELI Group, Ikulu, Dar es Salaam tarehe 29 Machi, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Mkurugenzi na Mmiliki wa DANIELI Group Bw. Giacomo Mareschi-Danieli, Ikulu, Dar es Salaam tarehe 29 Machi, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Balozi wa Italia nchini Tanzania Mheshimiwa Giuseppe Sean Coppola pamoja na ujumbe kutoka DANIELI Group, Ikulu, Dar es Salaam tarehe 29 Machi, 2026.






Top News