Serikali ya Mkoa wa Dodoma imewataka wafanyabiashara, wawekezaji, washauri wa kodi na wananchi kuendelea kushirikiana na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwa kuzingatia sheria za kodi ili kuongeza mapato ya Serikali na kuchochea maendeleo ya Taifa.

Wito huo umetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Chamwino, Mhe. Janeth Mayanja, aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Dodoma katika maadhimisho ya miaka 30 ya TRA na hafla ya utoaji wa Tuzo za Mheshimiwa Rais kwa Walipakodi Bora,Julai 1, 2026 Jijini Dodoma.

Mhe. Mayanja amesema wafanyabiashara wanapaswa kusajili biashara zao kwa mujibu wa sheria, kutunza kumbukumbu sahihi za biashara, kuwasilisha ritani za kodi kwa wakati na kulipa kodi kwa hiari, kwa wakati na kwa usahihi.

Aidha, amewahimiza kutumia mifumo rasmi ya Serikali katika kufanya malipo, kutumia mashine za EFD ipasavyo na kutoa risiti halali kwa kila mauzo, huku akiwataka wananchi kudai risiti kila wanaponunua bidhaa au huduma na kuepuka vitendo vya ukwepaji wa kodi vinavyokwamisha maendeleo ya Taifa.

Amesema ushirikiano huo utawezesha Serikali kuongeza mapato na kutekeleza miradi mingi zaidi ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi, huku Mkoa wa Dodoma ukiendelea kushirikiana kwa karibu na TRA kuhakikisha mazingira ya biashara yanakuwa rafiki na changamoto za walipakodi zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati.

Kwa upande wake, Kaimu Meneja wa TRA Mkoa wa Dodoma, John Njau, amesema maadhimisho ya miaka 30 ya TRA ni fursa ya kutafakari mafanikio yaliyopatikana tangu kuanzishwa kwa mamlaka hiyo mwaka 1996, ikiwemo maboresho ya mifumo ya ukusanyaji wa mapato, matumizi ya teknolojia za kidijitali na utoaji wa huduma bora kwa walipakodi.

Njau amesema mafanikio hayo yamechangiwa na ushirikiano wa walipakodi na wadau mbalimbali, huku akiwapongeza walipakodi wanaotekeleza wajibu wao kwa hiari na waliotunukiwa Tuzo za Rais kwa Walipakodi Bora kwa kuwa mfano wa kuigwa katika kujenga uchumi wa Taifa.

Naye Mwenyekiti wa Washauri wa Kodi Mkoa wa Dodoma, CPA Dkt. Lucas Webie, amewataka wafanyabiashara kuacha kuiangalia TRA kama adui, akisema mamlaka hiyo hutoa nafasi ya kusikiliza changamoto za walipakodi na kuweka utaratibu wa ulipaji wa kodi kwa awamu, huku akisisitiza kuwa mapato ya kodi ndiyo msingi wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo nchini.








▪️ Waziri Mavunde akutana na mwekezaji wa kiwanda cha kuzalisha goroli za chuma

▪️ Kiwanda hicho kinatarajiwa kujengwa Buzwagi Special Economic Zone, Kahama

▪️ Oriental Casting and Forging Ltd ya China yajipanga kuwekeza nchini

▪️ Serikali yalenga kupunguza utegemezi wa bidhaa za migodini kutoka nje

▪️ Tanzania yajipanga kuwa kitovu cha uzalishaji na usambazaji wa bidhaa za migodini Afrika

Dar es Salaam: Tanzania imeanza kujipanga kuwa kitovu cha uzalishaji na usambazaji wa bidhaa za migodini barani Afrika, baada ya Serikali kuvutia uwekezaji wa viwanda vitakavyozalisha bidhaa muhimu zinazotumiwa na wachimbaji wakubwa na wadogo nchini.

Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, leo amekutana na Mkurugenzi Mkuu na mmiliki wa kampuni ya Oriental Casting and Forging Ltd ya China, Hou Songcun, kujadiliana kuhusu uwekezaji wa kiwanda cha kuzalisha goroli za chuma zinazotumika kusaga miamba ya madini katika shughuli za uchenjuaji.

Mavunde amewakaribisha wawekezaji hao kujenga kiwanda hicho katika eneo la Buzwagi Special Economic Zone lililopo Kahama, Shinyanga, ambalo Serikali imelitenga kwa ajili ya uwekezaji wa viwanda vinavyohudumia Sekta ya Madini.
Amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeweka mazingira mazuri ya uwekezaji na sasa inalenga kuvutia viwanda vitakavyozalisha bidhaa za migodini ndani ya nchi, badala ya kuendelea kutegemea uagizaji kutoka nje.

“Lengo letu ni kuona wachimbaji wakubwa na wadogo hapa nchini wanapata bidhaa nyingi za kuzalisha madini bila kutegemea sana uagizaji wa bidhaa hizo kutoka nje ya nchi,” amesema Mavunde.

Amesema Tanzania ina nafasi kubwa ya kuwa kitovu cha uzalishaji na usambazaji wa bidhaa za migodini barani Afrika kutokana na ukuaji wa Sekta ya Madini, mahitaji makubwa ya bidhaa hizo na mazingira bora ya uwekezaji yaliyowekwa na Serikali.

Kwa mujibu wa Mavunde, uwekezaji wa viwanda vinavyohudumia Sekta ya Madini utaongeza ajira, kupunguza gharama za uzalishaji kwa wachimbaji, kuimarisha mnyororo wa thamani wa madini na kuongeza ushiriki wa viwanda vya ndani kwenye uchumi wa madini.
Amesema Serikali itaendelea kuvutia na kuunga mkono wawekezaji wanaolenga kujenga viwanda vinavyounganisha uchimbaji wa madini na uzalishaji wa bidhaa zinazotumika migodini, ili kuongeza manufaa ya sekta hiyo kwa uchumi wa Taifa.

Kwa upande wake, Hou Songcun amesema kampuni yake iko tayari kufanya uwekezaji mkubwa nchini kwa kuwa Tanzania ina mazingira rafiki ya uwekezaji na Sekta ya Madini inaendelea kukua kwa kasi.

Amesema uzalishaji wa bidhaa za migodini ndani ya Tanzania utarahisisha upatikanaji wa vifaa hivyo kwa wachimbaji, kupunguza utegemezi wa bidhaa zinazoagizwa kutoka nje ya nchi na kuongeza uhakika wa upatikanaji wa bidhaa muhimu katika shughuli za uchimbaji.

Kiwanda hicho kinatarajiwa kuongeza uwezo wa Tanzania kuzalisha bidhaa muhimu za migodini ndani ya nchi, kuimarisha viwanda vinavyohudumia Sekta ya Madini na kuiweka Kahama katika nafasi muhimu ya uzalishaji wa bidhaa za migodini kwa soko la ndani na la kikanda.

-Watuhumiwa 188 washikiliwa wakuhusishwa na dawa hizo,sheria kuchukua mkondo wake


Na Said Mwishehe,Michuzi TV

MAMLAKA ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imefanya operesheni maeneo mbalimbali nchini na kufanikiwa kukamata tani 22.6 za dawa za kulevya, lita 30.5 na kilogramu 19.94 za dawa tiba zenye asili ya kulevya. 

Pia, imeteketeza ekari 228.5 za mashamba ya bangi pamoja na tani 3.3 za bangi na mirungi huku ikiyashikilia magari sita, bajaji mbili na pikipiki 33 zilikamatwa kuhusiana na uhalifu huo wakati watuhumiwa 188 wamekamatwa kwa hatua za kisheria.

Akizungumza jijini Dar es Salaam leo Julai 2,2026 Kamishina Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Aretas Lyimo amesema operesheni hiyo imefanyika kati ya Mei na Juni mwaka huu.

Amesema operesheni zilizofanyika Dar es Salaam zilifanikisha ukamataji wa kilogramu 19.94 za bidhaa zilizotambulishwa kama virutubisho vya lishe aina ya AFA CELL (Moringa Extract) katika eneo la mizigo inayosafirishwa kwenda nje ya nchi kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere. 

“Baada ya kufanyiwa uchunguzi wa maabara, ilibainika kuwa bidhaa hizo zilikuwa na kiambata cha dawa tiba yenye asili ya kulevya aina ya Prazepam. Bidhaa hizo ziliingizwa nchini kutoka Malaysia na zilikuwa zinaandaliwa kusafirishwa kwenda Barbados katika visiwa vya Karibiani. 

Amefafanua katika tukio hilo watuhumiwa Agustino Metusela Ismaely (30), mkazi wa Kimara; Zamia Harid Upunda (23), mkazi wa Bungoni, Ilala; na Habiba Ally Mziga (54), mkazi wa Mbezi Makonde walikamatwa.

“Prazepam ni dawa tiba yenye asili ya kulevya iliyopo katika kundi la benzodiazepine inayotumika kutibu magonjwa mbalimbali ikiwemo wasiwasi, msongo wa mawazo na kukosa usingizi. Endapo dawa hizi zitatumika kiholela au bila maelekezo ya daktari zinaweza kusababisha uraibu, kuharibu mfumo wa fahamu, mfumo wa upumuaji, kupoteza fahamu na hata kifo.”

Katika operesheni nyingine iliyofanyika mtaa wa Manyanya, Kinondoni, amesema zilikamatwa kilogramu 34.87 za mirungi iliyokuwa ikisafirishwa kwa kutumia gari aina ya Fuso lenye namba za usajili T 490 ECM kutoka Tarakea, mkoa wa Kilimanjaro. 

Amesema Mirungi hiyo iliyotokea nchini Kenya ilikuwa imefichwa kwa kuchanganywa na matenga ya nyanya ili kuficha uhalisia wa mzigo huo. Baada ya kufikishwa Dar es Salaam, ilishushwa katika eneo la kituo cha mafuta kilichopo mtaa huo kabla ya kuanza kusambazwa kwa kutumia usafiri wa bajaji yenye namba za usajili MC 361 CZV.

“Katika tukio hilo, walikamatawa watuhumiwa Mohamed Omary Mohamed (24), utingo na mkazi wa Tandale; Suleman Omary Suguti (34), dereva wa gari hilo na mkazi wa Tarakea, Rombo; na Deo Paschal Maratua (32), dereva wa bajaji na mkazi wa Tandale kwa Mtogole. 

“Mtuhumiwa Husseni Jumaa

Salimu (52), mkazi wa Dar es Salaam, ambaye anadaiwa kuwepo Nairobi, Kenya, anatafutwa kuhusiana na tukio hilo.”

Aidha amesema katika operesheni iliyofanyika eneo la ukaguzi wa mizigo la Bandari ndogo ya boti zinazotoa huduma kati ya Dar es Salaam na Zanzibar, zilikamatwa gramu 972.05 za mirungi zilizokuwa zikisafirishwa na mtuhumiwa Kalsam Abdurahman Sebbi (43), raia wa Kenya mwenye makazi yake Mombasa. 

Wakati wilayani Kigamboni mkoani Dar es Salaam  zilikamatwa gramu 162.48 za heroin zilizomuhusisha mtuhumiwa Omary Miraji Mbonaeni.

Pia mkoani Arusha, zilikamatwa kilogramu 106.04 za dawa za kulevya aina ya mirungi zilizokuwa zikisafirishwa kwa kutumia gari aina ya Toyota Premio lenye namba za usajili T 853 ECX. 

Kamishina Jenerali Lyimo amesema katika tukio hilo, alikamatwa mtuhumiwa Goodluck Erasto Nyakaselula (35), mkazi wa Mbezi Beach, Dar es Salaam, ambaye ni mtaalam wa picha za kitabibu (Radiographer) katika Hospitali ya Ocean Road ya jijini Dar es Salaam.

Aidha, wilayani Same mkoani Kilimanjaro, eneo la kituo cha mabasi yaendayo mikoani, zilikamatwa kilogramu 240 za mirungi zikiwa zimefichwa ndani ya mabegi ya nguo. Katika tukio hilo, walikamatwa watuhumiwa Irene Obedi Sule na Eliasi Obedi Sule.

Kufuatia operesheni zilizofanyika katika mikoa mingine nchini, zilikamatwa tani 19.5 za bangi, tani 2.6 za mirungi, gramu 11.63 za heroin na kilogramu 40 za skanka. 

Aidha, tani 3.3 za bangi na mirungi pamoja na ekari 228.5 za mashamba ya bangi ziliteketezwa katika wilaya za Chamwino mkoa wa Dodoma, kijiji cha Mwengei kilichopo wilaya ya Kilwa mkoa wa Lindi na katika vijiji vya Busekeseke na Miembeni vilivyopo wilaya ya Sengerema na Geita.




Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga (Mb), akipokelewa na Mkuu wa Mtandao wa Matawi na Mauzo wa Benki ya NMB, Donatus Richard, alipotembelea banda la benki hiyo katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam yanayoendelea katika Viwanja vya Saba Saba. 

Katika ziara hiyo, Waziri Kapinga alipewa maelezo kuhusu suluhisho mbalimbali za kibenki zinazochochea ukuaji wa biashara, ujumuishaji wa kifedha na mageuzi ya uchumi wa kidijitali nchini.






 Na Said Mwishehe,Michuzi TV


MAMLAKA ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya imesema imebaini uwepo wa vinywaji hasa Energy drinks nchini viambata vya kemikali ya THC ambayo hupatikana kwenye dawa za kulevya aina ya bangi ambavyo vilikuwa vinauzwa katika duka la Village Supermarket lililopo jijini Dar es Salaam.

Akizungumza leo Julai 2,2026 jijini Dar es Salaam wakati akitoa taarifa kuhusu operesheni zilizofanywa na Mamlaka hiyo katika kipindi cha Mei na Juni 2026, Kamishina Jenerali wa Mamlaka hiyo Aretas Lyimo amesema kupitia uchunguzi uliofanywa kwa kushirikiana na mamlaka nyingine wamebaini uwepo wa vinywaji vya Energy ambavyo vimechanganywa na bangi.

“Kwa kushirikiana na Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali (GCLA), Shirika la Viwango Tanzania (TBS) na Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) ulifanyika ukaguzi na uchunguzi wa bidhaa katika duka la bidhaa lijulikanalo kama “village supermarket” la jijini Dar es Salaam .

“Katika uchunguzi huo tumebaini uwepo wa vinywaji hususan “energy drinks” zenye viambata vya kemikali ya THC ambayo hupatikana kwenye dawa za kulevya aina ya bangi,”amesema

Amefafanua jumla ya kopo 122 zenye ujazo wa mililita 250 kila moja, sawa na lita 30.5 zenye chapa ya “TRIP” zilikamatwa. Watuhumiwa Syed Abdul Bast (43) raia wa Pakistan na Dhirendra Kumar Gorodhan (45), mtanzania mwenye asili ya Asia walikamatwa katika tukio hilo.

“THC ni kemikali inayopatikana kwenye dawa za kulevya aina ya bangi ambayo, ina madhara mbalimbali kwa mtumiaji ikiwemo, kuamsha magonjwa ya akili, kubadili utendaji kazi wa mfumo wa fahamu, kuchochea vitendo vya kihalifu ikiwemo wizi, unyang`anyi, ukatili na kuchochea matumizi ya dawa nyingine za kulevya.”

Kutokana na kubaini uwepo wa vinywaji hivyo Kamishina Jenerali Lyimo amesema Mamlaka hiyo kwa kushirikiana na mamlaka nyingine watafanya operesheni ya kuchunguza bidhaa katika maduka yote ili kuhakikisha bidhaa zilozopo ziko salama na hazina viashiria vya dawa za kulevya.

Alipoulizwa vinywaji vya Energy vilivyokutwa vimechanganywa na bangi zimetengenezwa wapi,amejibu vimetengenezwa katika viwanda vya nje ya Tanzania na vimeingizwa nchini kinyemela na hata katika karatasi zake waliotengeneza hawakuandika uwepo wa kemikali hizo.



Na Mwandishi Wetu

Dar es Salaam. Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imeendelea kutoa huduma mbalimbali kwa waandishi wa habari, wadau wa sekta ya habari na wananchi kupitia banda lake lililopo katika Kijiji cha Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwenye Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba).

Huduma zinazotolewa ni pamoja na ugawaji wa vitambulisho vya ithibati kwa waandishi wa habari waliokidhi vigezo kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, usajili wa waandishi wa habari, marekebisho ya taarifa za usajili pamoja na utoaji wa elimu kuhusu majukumu na huduma mbalimbali zinazotolewa na Bodi hiyo.

JAB imesema ushiriki wake katika maonesho hayo unalenga kusogeza huduma karibu na wananchi na wadau wa sekta ya habari, ili kurahisisha upatikanaji wa huduma pamoja na kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa ithibati na usajili wa waandishi wa habari nchini.

Bodi hiyo imewahimiza waandishi wa habari na wadau wengine kutumia fursa ya maonesho hayo kupata huduma kwa haraka na kwa ukaribu, huku ikieleza kuwa huduma hizo zinaendelea kutolewa pia katika Makao Makuu ya JAB.

Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam yanaendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Barabara ya Kilwa, yakihusisha taasisi mbalimbali za umma na binafsi zinazowasilisha huduma na bidhaa zao kwa wananchi.
















Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro imewakumbusha wamiliki na madereva wa magari ya utalii kuwa makini , kuhakikisha magari yao yapo salama na kuzingatia sheria na taratibu za maeneo ya hifadhi hasa katika kipindi hiki cha msimu mkubwa wa utalii (High Season).

Taarifa iliyotolewa na Mamlaka hiyo imeeleza kuwa ni muhimu madereva na wamiliki wa magari ya kubeba watalii kuhakikisha wanatengeneza magari hayo ipasavyo, kuyakagua mara kwa mara na kuwa na madereva makini na wenye weledi wa kutosha wanapoendesha magari hayo..

“Tumeanza msimu mpya wa utalii, tunawakumbusha na kuwasisitiza wadau wote katika mnyororo wa utalii kuchukua hatua madhubuti ili kuhakikisha usalama wa watalii na watumiaji wengine wa barabara katika maeneo ya hifadhi unakuwa wa uhakika”,ilisema taarifa hiyo.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa uongozi wa Hifadhi ya Ngorongoro umejipanga kuendelea kutoa huduma zote muhimu kwa kuzingatia ubora na wakati sambamba na kutoa elimu ya mara kwa mara kwa madereva wa magari yanayobeba watalii na magari yanayobeba watu wengine wanaoishi ndani ya hifadhi kwa lengo la kuhakikisha usalama wa kila mtu unalindwa.

Uzoefu unaonesha kuwa katika msimu wa watalii wengi baadhi ya kampuni hutumia magari yasiyokuwa na ubora na baadhi ya madereva kutokuwa na uzoefu wa kutosha kuendesha watalii hifadhini hali inayosababisha changamoto kwa Watalii.


Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), akiteta jambo na Waziri wa Rasilimali Madini, Nishati, Viwanda, Biashara na Utalii wa Jamhuri ya Burundi Mhe. Hassan Kibeya, baada ya kumalizika kwa Mkutano Mkuu wa 26 wa Wanahisa wa Taasisi ya Bima ya Maendeleo ya Biashara na Uwekezaji Afrika (ATIDI), uliofanyika jijini Nairobi, Kenya.

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), akichangia wakati wa Mkutano Mkuu wa 26 wa Wanahisa wa Taasisi ya Bima ya Maendeleo ya Biashara na Uwekezaji Afrika (ATIDI), uliofanyika jijini Nairobi, Kenya.

 Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), akifuatilia mawasilisho mbalimbali wakati wa Mkutano Mkuu wa 26 wa Wanahisa wa Taasisi ya Bima ya Maendeleo ya Biashara na Uwekezaji Afrika (ATIDI), uliofanyika jijini Nairobi, Kenya.

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), akipitia nyaraka za Mkutano Mkuu wa 26 wa Wanahisa wa Taasisi ya Bima ya Maendeleo ya Biashara na Uwekezaji Afrika (ATIDI), uliofanyika jijini Nairobi, Kenya.

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) (katikati), akiteta jambo na Kaimu Kamishna, Idara ya Uendelezaji Sekta ya Fedha, Wizara ya Fedha Bi. Dionisia Mjema (kulia) na Naibu Kamisha wa Bima, Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) na Mjumbe wa Bodi ya Taasisi ya Bima ya Maendeleo ya Biashara na Uwekezaji Afrika (ATIDI) Bi. Khadija Issa Said, baada ya kumalizika kwa Mkutano Mkuu wa 26 wa Wanahisa wa Taasisi ya Bima ya Maendeleo ya Biashara na Uwekezaji Afrika (ATIDI), uliofanyika jijini Nairobi, Kenya.


Baadhi ya washiriki wa mkutano wakifuatilia mawasilisho mbalimbali yakiendelea wakati wa Mkutano Mkuu wa 26 wa Wanahisa wa Taasisi ya Bima ya Maendeleo ya Biashara na Uwekezaji Afrika (ATIDI), uliofanyika jijini Nairobi, Kenya.


Watumishi wa Wizara ya Fedha, wakifuatilia mawasilisho wakati wa Mkutano Mkuu wa 26 wa Wanahisa wa Taasisi ya Bima ya Maendeleo ya Biashara na Uwekezaji Afrika (ATIDI), uliofanyika jijini Nairobi, Kenya.


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Kenya, Prof. Kithure Kindiki, akifafanua jambo, wakati wa majadiliano, katika Mkutano Mkuu wa 26 wa Wanahisa wa Taasisi ya Bima ya Maendeleo ya Biashara na Uwekezaji Afrika (ATIDI), uliofanyika jijini Nairobi, Kenya.


Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) (wa tatu kutoka kulia), Kaimu Kamishna, Idara ya Uendelezaji Sekta ya Fedha, Wizara ya Fedha Bi. Dionisia Mjema (wa pili kutoka kulia) na Naibu Kamisha wa Bima, Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) na Mjumbe wa Bodi ya Taasisi ya Bima ya Maendeleo ya Biashara na Uwekezaji Afrika (ATIDI) Bi. Khadija Issa Said (wa tatu kutoka kushoto), wakiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Wizara ya Fedha baada ya kumalizika kwa Mkutano Mkuu wa 26 wa Wanahisa wa Taasisi ya Bima ya Maendeleo ya Biashara na Uwekezaji Afrika (ATIDI), uliofanyika jijini Nairobi, Kenya.


Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) (wa tatu kutoka kulia), Kaimu Kamishna, Idara ya Uendelezaji Sekta ya Fedha, Wizara ya Fedha Bi. Dionisia Mjema (wa tatu kutoka kushoto), wakiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Wizara ya Fedha baada ya kumalizika kwa Mkutano Mkuu wa 26 wa Wanahisa wa Taasisi ya Bima ya Maendeleo ya Biashara na Uwekezaji Afrika (ATIDI), uliofanyika jijini Nairobi, Kenya.

 

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Nairobi, Kenya)

 

Na Victor Masangu, Pwani

Serikali mkoani Pwani imeipongeza Mamlaka ya mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Pwani kwa kuweza kuwa na mipango madhubuti katika  kuweka mazingira rafiki na mazuri  ya  ukusanyaji wa mapato ambayo yameweza kusaidia kwa kiasi kikubwa katika kuleta mabadiliko chanya katika kuwezesha  utekelezaji wa  miradi mbali mbali ya maendeleo.

 Hayo yamebainishwa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Pwani Pili Mnyema wakati wa halfa ya kilele cha maadhimisho ya miaka 30 ya TRA ambapo katika ngazi ya Mkoa yalifanyika katika ukumbi wa shule ya uongozi Mwalimu Juliasi Nyerere Wilaya ya Kibaha  na kuwakutanisha  walipa kodi mbali mbali pamoja na  wadau wa   maendeleo, wananchi na viongozi wa viongozi wa dini.

Katika kilele cha maadhimisho hayo  ambayo yalikuwa ya aina yake yalikwenda sambamba na kufuatilia matangazo yaliyokuwa yanarushwa  moja kwa moja kufuatilia halfa ya utoaji wa tuzo za walipa kodi bora  mbali mbali Tanzania  ambazo zilikuwa zinatolewa na mgeni rasmi Rais Dkt. Samia Suluhu Hasssan  Jijini Dar es Salaam.

Katibu Tawala huyo amesema kwamba  TRA Mkoa wa Pwani wamekuwa mstari wa mbele katika suala zima la ukusanyaji wa mapato ikiwa sambamba na kutoa elimu ya kutosha kwa wafanyabiashara mbali mbali ambayo yameweza kuwasaidia walipa kodi kuweza kufahamu umuhimu wa kulipa kodi kwa hiari hali amabyo imeweza kuleta tija zaidi ya kuongeza kazi ya ukusanyaji.

"Nawapongeza sana TRA Mkoa wa Pwani kwa kuweza kutimiza miaka 30 tangu kuanzishwa kwake maana haikuwa safari nyepesi mmeweza kuvuka milima na mabonde kwa hali na mali kwa hiyo kwa upande wangu nawapongeza sana na mzidi kuendelea kukusanya mapato kwa ajili ya kuweza kuisaidia serikali kupata mapato yake kihalali ambayo yatakwenda katika kusaidia katika kutekeleza miradi mbali mbali ya maendeleo."amebainisha Katibu Tawala.

Kwa upande wake Kaimu Meneja wa Mamlaka ya mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Pwani  Salim Makame  amesema kwamba lengo lao kubwa  ni kuzidi  kuendelea kushirikiana  bega  kwa bega na walipa kodi wote  na kuwawekea mazingira mazuri  ambayo yataweza kuwasaidia katika kutekeleza majukumu yao ipasavyo.

"Tumetimiza miaka 30 ya TRA tangu kuanzishwa kwake kwa hiyo kitu kikubwa sisi tutaendelea kushirikiana bega kwa bega na wadau  pamoja na walipa kodi na kwamba kitu kikubwa zaidi tunaomba ushirikiano wenu ambao utaweza kutusaidia kwa upande wetu katika suala zima la ukusanyaji wa mapato kwa maendeleo ya Taifa letu hasa katika kipindi hiki tunapoanza mwaka mpya wa fedha ,"amebainisha Makame.

Aidha Makame amempongeza kwa dhati Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuweza kupambana  kwa hali na mali katika kuwahudumia wananchi wa Tanzania na kuahidi kuyatekeleza maelekezo  na maagizo mbali mbali ambayo yametolewa  na Rais na kwamba watayafanyia kazi ili  kuwa na TRA iliyobora zaidi katika utekelezaji wa majukumu yake.

Mamlaka ya mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Pwani katika kuadhimisha  kilele cha miaka 30  imeweza kufanya mambo mbali mbali ikiwemo kutoa msaada wa vifaa mbali mbali kwa wafanyabiashara, mama lishe, kutoa elimu ya mlipa kodi, pamoja na kukutana na wadau na walipa kodi ili kuweka mikakati ya pamoja ambayo  itasaidia katika ukusanyaji wa kodi  kwa hiari kwa maendeleo ya Taifa.





Top News