Waswahili husema "Dunia ni jumba la maajabu  " Ngorongoro haiishiwi maajabu , Ni kama vile lile fukuo la kufukulia maajabu ndani ya hifadhi ya eneo la Ngorongoro limefukuliwa, hii inatokana na enzi mpya za msimu kwa waongoza utalii (Tour Guide) nane kushiriki kwenye fainali za Safari Field Challenge kwa mwaka 2026 zitakazofanyika Ngorongoro 

Mamlaka ya Hifadhi ya eneo la Ngorongoro inadhamini mashindano hayo ambapo waongoza utalii wanaoshiriki shindano walipatikana kwa kufanyiwa mchujo na kupatikana washindi nane (08) ambao katika shindano hilo watapita kwenye vivutio ambavyo ni maajabu ya kustaajabisha na kutambua uwezo wao katika umahiri wa maarifa, ubinifu, ustahamilifu,  akili na uwezo wao wa kukabiliana na vikwazo katika safari za kitalii mbugani.

Akizungumza kwa niaba ya Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi Ngorongoro, Kamishna Msaidizi mwandamizi anayesimamia huduma za Utalii na Masoko Mariam Kobelo ameleza kiwa shindano hilo litatumika kuionesha dunia kuwa  Ngorongoro sio Kreta pekee bali asili, utamaduni, urithi, wanyamapori na pumzi ya kwanza ya Nyumbu wahamao zinakutana sehemu moja.

“Waongoza watalii ni mabalozi wetu wazuri katika huduma za utalii, kupitia Safari Field Challenge watapata fursa ya kujua na kuyazungumza maajabu ya Ngorongoro”, alisema Kamishna Mariam

Habari njema kwa ulimwengu kuhusu Ngorongoro ni pamoja na uelekeo wake wa kuwa Bustani ya Eden kutokana na kubeba historia ya kuumbwa kwa binadamu na vilivyoutawala ulimwengu.

Safari Field Challenge imeandaliwa na  chama cha Waongoza Utalii (TTGF) kwa kushirikiana na Azam Media na Wadau wengine wa Utalii.





JAMHURI ya Muungano wa Tanzania imesisitiza matumizi ya Akili Unde (Artificial Inteligence – AI) ikiwa ni moja ya nyenzo muhimu na ya kisasa katika kukuza mtangamano na kuharakisha maendeleo katika Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kupitia sekta mbalimbali ikiwemo Kilimo, Elimu, Viwanda, Afya na Biashara.

Rai hiyo imetolewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Mahmoud Thabit Kombo katika Kongamano la Nne la Sayansi, Teknolojia na Ubunifu la Jumuiya ya Afrika Mashariki (4th EAC Regional Science, Technology and Innovation Conference) lililoandaliwa na Kamisheni ya Sayansi na Teknolojia ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EASTECO) kwa kushirikiana na Bazara la Vyuo Vikuu la Jumuiya ya Afrika Mashariki (IUCEA), linalofanyika jijini Kigali, Rwanda kuanzia tarehe 30 Machi – hadi 1 Aprili 2026.

Waziri Kombo akizungumza katika Kongamano hilo lililowakutanisha viongozi wa ngazi za juu Serikalini kutoka nchi wanachama wa EAC, wabunifu, wanataaluma, wanadiplomasia na wadau wa maendeleo, amesisitiza nafasi ya akili unde katika kuongeza ufanisi na tija ikiwemo kuboresha utoaji wa huduma za umma na kuimarisha ushindani wa kiuchumi ndani ya Jumuiya na kwenye soko la kimataifa.

Akizungumzia mchango wa Tanzania, Waziri Kombo alieleza kuwa, Tanzania chini ya uongozi wa Rais Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeweka kipaumbele katika kukuza sekta za Teknolojia, Uchumi wa Kidijitali na Ubunifu kama nguzo muhimu za agenda ya maendeleo ya taifa na Dira ya Maendeleo ya 2050. Alisisitiza kuwa mwelekeo huo unalenga kuchochea maendeleo jumuishi, kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi na kuinua ustawi wa jamii hususan vijana.

Katika kuimarisha ushirikiano wa kikanda, Waziri Kombo amehimiza nchi wanachama kuongeza juhudi za pamoja katika utafuataji wa rasilimali fedha za kuendesha programu mbalimbali ikiwemo utafiti na ujenzi wa miundombinu ya kidijitali, kubadilishana maarifa, kukuza ubunifu wa ndani na kuendeleza miradi ya pamoja ya teknolojia ili kujenga uthabiti wa kiuchumi na kijamii katika Jumuiya.

Mbali na hayo Waziri Kombo aligusia umuhimu wa kuweka mifumo thabiti ya sera na udhibiti na utoaji elimu ili kuhakikisha matumizi salama na yenye maadili ya Akili Unde. Aliongeza kuwa pasipo kuwa na usimamizi madhubuti wa teknolojia hiyo inaweza kuongeza changamoto katika jamii ikiwemo tishio la usalama na kukithiri kwa tofauti ya kiuchumi.

Katika mkutano huo uliofanyika chini ya kauli mbiu isemayo “Matumizi ya Akili Unde kwa ajili ya Afrika Mashariki yenye Ustahimilivu, Jumuishi na Ubunifu” (“Harnessing Artificial Intelligence for a Resilient, Inclusive and Innovative East Africa”) ujumbe wa Tanzania uliongozwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Mahmoud Thabit Kombo aliyeambatana na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. Prof. Adolf Mkenda, Katibu Mkuu Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Bw. Mohammed Khamis Abdulla, Kaimu Katibu Mkuu anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Said Shaib Mussa, Maafisa Waandamizi wa Wizara na Taasisi za Serikali pamoja na Wanataaluma kutoka Taasisi za mbalimbali za Elimu ya Juu nchini.



“JK na Dar City Afrika Kusini”
Rais Mstaafu Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Jopo la Wazee la Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC Panel of Elders - POE), na Mwakilishi wa Ngazi ya Juu wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika katika juhudi za kutatua mgogoro wa Sudan Kusini, amekutana leo na timu ya mpira wa kikapu ya Dar City inayoshiriki Michuano ya Ligi ya Mpira wa Kikapu Afrika (Basketball Africa League (BAL) 2026, inayoendelea jijini Pretoria, Afrika Kusini.

Katika mazungumzo na timu hiyo iliyoambatana na Rais wa Shirikisho la Mpira wa Kikapu Tanzania (TBF), Hasheem Thabit pamoja na Viongozi wengine kutoka Serikalini, Rais Mstaafu Dkt. Kikwete ameipongeza Timu ya Dar City kwa kufikia hatua hiyo muhimu ya mashindano, akieleza kuwa mafanikio hayo ni ishara ya kukua kwa kiwango cha mpira wa kikapu nchini Tanzania.

Aidha, amewatia moyo na kuwapa ari wachezaji ya kupambana katika mchezo wao mmoja uliosalia kabla ya kufika fainali, akisisitiza umuhimu wa nidhamu, kujituma na kujiamini wanapoingia uwanjani. "Kwa hatua mliyofikia, nina imani kabisa mnaweza kutinga fainali na hatimaye kubeba kombe hili, labda itokee miujiza", alisema Dkt. Kikwete akizungumza na wachezaji hao.

Rais Mstaafu Dkt. Kikwete, ambaye amewahi kuwa mlezi wa Shirikisho la Mpira wa Kikapu Tanzania (TBF) huku akiwa mstari wa mbele katika kuendeleza mchezo huo wakati wa uongozi wake, ametumia fursa hiyo pia kutoa pongezi kwa dhati kwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uwekezaji mkubwa unaofanyika katika sekta ya michezo nchini. Aidha, ameipongeza Wizara yenye dhamana ya kusimamia Michezo pamoja na Shirikisho la TBF kwa kusimamia vizuri maendeleo ya mpira wa kikapu, huku akibainisha kuwa mafanikio ya timu ya Dar City ni mojawapo ya matunda ya Serikali kuwekeza katika michezo.

Mheshimiwa Dkt. Kikwete yupo nchini Afrika Kusini kwa ziara ya kikazi ambapo amekutana na Rais wa Jamhuri ya Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa, kama sehemu ya kutekeleza majukumu yake ya kikanda akiwa kama Mwenyekiti wa Jopo la Wazee la SADC, pamoja na jukumu lake jipya chini ya Umoja wa Afrika la kusaidia kutafuta suluhu ya mgogoro wa Sudan Kusini.

Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Majisafi na usafi wa Mazingira Songea SOUWASA, Mhandisi Patrick Kibasa, amesema kuwa mradi mkubwa wa maji unaotekelezwa katika Manispaa ya Songea unaendelea vizuri, licha ya changamoto chache zilizojitokeza.

Mradi huo ni sehemu ya mpango wa Serikali wa kuboresha huduma za majisafi na usafi wa mazingira katika miji 28 nchini, ukilenga kumaliza changamoto ya maji kwa wakazi wa Songea.

Ameyasema hayo  Machi 30, 2026, wakati wa ziara ya Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Taifa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Mjumbe wa Kamati Kuu, Maganya Fadhili Rajabu, aliyefika kutembelea maendeleo ya mradi huo wa kimkakati mkoani Ruvuma.

Kibasa ameeleza kuwa mkataba wa utekelezaji wa mradi ulisainiwa Machi 10, 2022 kati ya Wizara ya Maji na kampuni ya China Civil Engineering Construction Corporation (CCECC), huku ujenzi ukianza rasmi Januari 2, 2024 na hadi sasa mradi umefikia asilimia 6.5 ya utekelezaji. 

Amesema mradi huo una thamani ya shilingi bilioni 145.77 unahusisha ujenzi wa kidaka maji katika Mto Njuga, mtambo wa kisasa wa kuchuja na kutibu maji wenye uwezo wa kuzalisha lita milioni 16 kwa siku, pamoja na matanki matatu ya kuhifadhi maji yenye ujazo wa lita milioni 9 kwa jumla.

Aidha, zaidi ya kilomita 60 za mabomba ya kusafirisha na kusambaza maji zinajengwa sambamba na ukarabati wa mtambo wa Matogoro ili kuongeza ufanisi wa huduma. Hatua zilizofikiwa ni pamoja na usanifu wa miundombinu, ujenzi wa matanki mawili katika maeneo ya Maji Wilaya na Chandamali, pamoja na ujenzi wa tanki la Mahilo lenye ujazo wa lita milioni 5 ambalo limefikia asilimia 70 ya utekelezaji.

Hata hivyo, Kibasa ameainisha changamoto ya mabadiliko ya chanzo cha maji kutoka bwawa lililopangwa awali kwenda Mto Njuga kutokana na sababu za kiufundi, hali iliyopunguza kasi ya utekelezaji wa mradi.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi wa CCM Taifa, Maganya Fadhili Rajabu amesisitiza wananchi kuwa na subira huku akiitaka jamii kushirikiana na Serikali ili kuhakikisha mradi unakamilika kwa mafanikio. 

Amesema Serikali chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan inaendelea kuchukua hatua madhubuti za kuboresha huduma za maji nchini, ikilenga kufikia upatikanaji wa maji kwa asilimia 100 katika maeneo ya mijini.

Mradi huo unatarajiwa kuondoa changamoto ya maji safi na salama kwa wakazi wa Songea na kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika eneo hilo.








TAASISI isiyo ya kiserikali ya Afya ya Mama Foundation imekabidhi mikoba ya vifaa vya kujifungulia wajawazito katika vituo vya afya vya Kimbiji na Mwasonga, wilayani Kigamboni, mkoani Dar es Salaam, ikiwa ni hatua ya kuunga mkono serikali chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, kuhakikisha uzazi salama.

Akizungumza katika hafla ya kukabidhi vifaa hivyo leo Mwenyekiti wa Bodi ya taasisi hiyo, Felister Bwana, alisema hatua hiyo inathibitisha dhamira ya pamoja ya kulinda maisha ya mama na mtoto mchanga kuhakikisha kila mwanamke anapitia ujauzito na kujifungua kwa heshima, salama na matumaini.

"Nchini Tanzania tumeshuhudia maendeleo ya kutia moyo katika afya ya uzazi kutokana na juhudi za serikali , wahudumu wa afya, washirika wa maendeleo na jamii kwa ujumla.Mafanikio haya yanatuonesha kushirikiana inawezekana,"amesema Felister.

Ameeleza,Afya ya Mama Foundation inatambua wanawake na watoto wachanga wengi wako katika hatari kwa sababu zinazozuilika hususan changamoto wakati wa ujauzito, kujifungua, kuchelewa kupata huduma, upungufu wa vifaa muhimu hasa katika maeneo yenye rasimilali chache.

"Ndiyo maana tumeamua kukabidhi vifaa hivi vya kujifungulia ambavyo vinaweza kuonekana rahisi lakini vinathamani kubwa kwani vinawakilisha maandalizi, usalama na huduma bora katika kujifungua, kupunguza hatari za maambukizi na kuwasaidia wahudumu wa afya kutoa huduma bora zaidi,"amesema Felister.

Amesema, vifaa hivyo pia vinatuma ujumbe muhimu kwa kila mama kuwa hayuko peke yake kwani afya yake na maisha yake ni muhimu.

"Napenda kutoa shukrani kwa Serikali ya Tanzania kwa uongozi wake endelevu na dhamira ya kuboresha afya ya mama na mtoto. Juhudi hizi ndiyo msingi unaowezesha taasisi kama hii kushirikiana na kuchangia maendeleo haya,"amebainisha.

Awali Mwanzilishi wa Afya ya Mama Foundation, Nkela Makoko, alisema taasisi hiyo inatambua umuhimu wa vifaa hivyo kwa wajawazito kwani baadhi wanashindwa kuvipata wakati wa kujifungua.

"Lengo letu kuu ni kusaidia huduma za mama na mtoto katika kipindi chote cha ujauzito, kujifungua na maendeleo yake baada ya kujifungua. Vifaa hivi vimetolewa na wadau wetu walio guswa na afya ya mama na mtoto,"ameeleza Nkela.

Ameishukuru serikali chini ya Rais Dk. Samia, kuboresha huduma za mama na mtoto hali inayopunguza athari za uzazi kabla, wakati na baada ya kujifungua.

Mganga wa Mfawidhi wa Kituo cha Afya Mwasonga, Miriam Issa, ameishukuru taasisi hiyo kwa kutoa vifaa hivyo kwa wajawazito ambavyo amesema ni mahitaji muhimu wakati wa kujifungua.

Wanufaika wa vifaa hivyo ambao ni wajawazito, wamesemavifaa hivyo ni zawadi muhimu kwao kwani baadhi yao wanapata changamoto ya kumudu mahitaji yote wakati wa kujifungua.

"Wajawazito tunapata shida unapofika wakati wa kujifungua. Tunashukuru Afya ya Mama Foundation kwa kutukumbuka kutupa vifaa hivi,"alisema Tachael Paul.








Ajali imetokea katika Mgodi wa Dhahabu wa Msasa uliopo Runzewe, Wilaya ya Bukombe mkoani Geita, baada ya sehemu ya eneo la uchimbaji kuporomoka na kufunika madarura manne yenye namba K 46A, 47A, 48A na 49A.

Kwa mujibu wa Ofisi ya Afisa Madini Mkazi – Mbogwe, madarura hayo yalikuwa yamefungwa tangu Machi 27, 2026 kwa ajili ya ukarabati, hata hivyo baadhi ya watu waliingia katika eneo hilo bila kufuata taratibu.


Taarifa imeeleza kuwa mvua kubwa zinazoendelea kunyesha zimechangia kulegea kwa udongo na kusababisha tukio hilo.


Jitihada za uokoaji zilifanyika na hakuna kifo kilichoripotiwa.


Tume ya Madini imewataka wachimbaji na wananchi kuzingatia taratibu za usalama migodini ili kuepusha ajali kama hizi.



Na said Mwishehe,Michuzi TV

MKURUGENZI Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa(TAKUKURU)Chrispian Chalamila amekabidhi ripoti ya utendaji kazi wa taasisi hiyo kwa Rais Dk.Samia Suluhu Hassan ambapo pia ilifuatilia matumizi ya rasilimali za umma katika utekelezaji wa miradi 1,864, ambapo miradi 913 ilibainika kuwa na kasoro.

Akizungumza leo MachI 30,2026 Ikulu jijini Dar es Salaam wakati akikabidhi ripoti hiyo ya TAKUKURU ya mwaka ya mwaka 2024/2025,Chalamila amesema kati ya miradi hiyo 913 yenye kasoro wakati miradi 66 imeanzishiwa uchunguzi.

Amesema idadi hiyo ni pungufu ikilinganishwa na miradi 92 iliyoanzishiwa uchunguzi mwaka 2023/24. “Idadi hii inaonesha kuwa miradi inayoanzishiwa uchunguzi inapunguahatua inayotokana na ufuatiliaji wa TAKUKURU katika utekelezaji wa miradi hiyo.

“Kwa ujumla, katika ufuatiliaji huu, tumebaini kuwepo kwa usimamizi dhaifu wa mikataba unaosababisha yafuatayo :Miradi kutekelezwa kwa kutozingatia matakwa ya mkataba husika,Wakandarasi kulipwa fedha kwa kazi ambazo hazikutekelezwa, kutokatwa kwa kodi ya zuio katika baadhi ya miradi.

“Pia ubora wa kazi na vifaa usioridhisha,kutozingatiwa kwa Sheria ya Ununuzi wa Ummaya Mwaka 2023; pamoja na Kufanyika kwa malipo - zaidi ya matakwa ya mkataba.

“Dosari zinazobainika katika ufuatiliaji wa matumizi ya rasilimali za umma katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo, zimekuwq zikijirudia.Nichukue fursa hii kuwakumbusha wote wenye dhamana ya kusimamia miradi hiyo wakiwemo makatibu wakuu,makatibu tawala na wakurugenzi wa halmashauri pamoja na taasisi za umma.”


NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

SEKTA binafsi imeelezwa kuwa nguzo muhimu katika kufanikisha malengo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo (FYDP IV), huku Serikali ikisisitiza umuhimu wa kuongeza ushiriki wake katika uwekezaji wa nishati ili kufikia uzalishaji wa megawati 70,000 ifikapo mwaka 2050.

Hayo yamebainishwa Machi 30, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa kongamano la kitaifa kuhusu ubia kati ya sekta ya umma na binafsi (PPP) katika sekta ya nishati, lililolenga kujadili nafasi ya sekta binafsi katika kuhakikisha upatikanaji wa nishati ya uhakika chini ya Mpango wa Nne wa Maendeleo.

Akizungumza katika kongamano hilo, Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Ubia kati ya sekta ya umma na sekta binafsi (PPPC), David Kafulila, alisema sekta binafsi ni mhimili muhimu katika utekelezaji wa mpango huo, ambao ni sehemu ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Alifafanua kuwa rasilimali za Serikali pekee, zikiwemo mapato ya kodi na mikopo, hazitoshi kufikia lengo la uzalishaji wa umeme unaotarajiwa kufikia takribani megawati 70,000 ifikapo mwaka 2050.

Kutokana na hali hiyo, alisisitiza umuhimu wa sekta binafsi kushiriki kikamilifu katika uwekezaji wa miradi ya uzalishaji na usafirishaji wa umeme ili kuongeza kasi ya maendeleo ya sekta hiyo.

Kafulila alieleza kuwa licha ya kuwepo kwa vikwazo vya kisheria vinavyozuia baadhi ya aina za ubia katika sekta ya usafirishaji wa umeme, Serikali imeanza hatua za majaribio kwa kushirikiana na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) pamoja na kampuni binafsi, ili kuanzisha mradi wa kwanza wa aina hiyo.

Aliongeza kuwa hatua hiyo inalenga kupima ufanisi wa ubia huo, sambamba na kutoa fursa ya kuboresha mifumo ya kisheria ili kuruhusu ushiriki mpana zaidi wa sekta binafsi katika siku zijazo.

Kwa upande wake, Balozi Modest Mero alisisitiza umuhimu wa kuimarisha maadili na mtazamo mpana miongoni mwa wadau wa sekta za umma na binafsi ili kuhakikisha rasilimali zinatumika kwa manufaa ya umma.

Alionya kuwa kutokuzingatia hilo kunaweza kusababisha maamuzi yanayoweka mbele maslahi binafsi badala ya maendeleo ya wananchi, akihimiza hatua za haraka zichukuliwe kukabiliana na changamoto za teknolojia na rasilimali.

Naye mtaalamu wa uchumi, Dkt. Avit Mushi, alisema sekta binafsi ina nafasi kubwa ya kuharakisha maendeleo kutokana na ufanisi wake, akisisitiza umuhimu wa taasisi na watumishi kuwa na mtazamo chanya wa kufanikisha malengo ya maendeleo ili kuongeza tija.







Na Said Mwishehe,Michuzi TV

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa(TAKUKURU) imesema imeendesha kesi 1,016 zikiwamo kesi mpya 755 zilizofunguliwa mwaka 2024/25 katika ngazi mbalimbali za Mahakama nchini.

Akizungumza leo Machi 30,2026 Ikulu jijini Dar es Salaam mbele ya Raos Dk.Samia Suluhu Hassan ,Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU Chrispin Chalamila wakati akikabidhi taarifa ya utendaji kazi wa taasisi hiyo 2024/2025 amesema katı ya kesi hizo mpya, 10 zimefunguliwa Mahakama Kuu Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi.

Amesema pia kesi 593 zimetolewa uamuzi Mahakamani,ambapo Jamhuri imeshinda kesi 483. Hilo ni ongezeko ikilinganishwa na kesi 440 zilizotolewa uamuzi na kesi 334 zilizoshinda mwaka 2023/2024.

Amesema kuwa kwa mwaka 2024/25, kiwango cha kushinda kesi ni asilimia 81.5. Kiwango hiki kimeongezeka I kilinganishwa na kiwango cha asilimia 76 kilichofikiwa mwaka 2023/24.

Wakati huo huo amesema kazi nyingine zilizofanyika ni uchunguzi wa majalada 169 yanayohusu tuhuma za ubadhirifu wa fedha ya mapato katika Halmashauri mbalimbali.

Amefafanua uchunguzi ulibaini Sh.bilioni 12.3 kilikusanywa kwa mashine za kukusanyiaushuru (POS) kupitia mfumo wa kielektroniki wa kurahisisha ukusanyaji wa mapato ya ndani pasipo kuwasilishwa benki.

“Kati ya majalada yaliyochunguzwa: majalada 32 yanaendelea na uchunguzi; majalada 39 yamewasilishwa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka kuomba kibali cha mashtaka na majalada mawiliyalipata kibali cha kufunguliwa mashtaka Mahakamani;

“Majalada 49 kesi zinaendelea Mahakamani; majalada nane watuhumiwa wamechukuliwa hatua za kinidhamu; na majalada 39 yalifungwa kutokana na kukosekana kwa ushahidi.Kupitia uchunguzi huu, TAKUKURU ilioko fedha Sh.bilioni moja na tunaendelea na uchunguzi ili kuhakikisha kuwa kiasi chote kilichofanyiwa ubadhirifu kinarejeshwa.”

Aidha amesema kupitia operesheni walizofanya uchunguzi wa TAKUKURU sababu za ubadhirifu kuendelea kufanyika kwenye ukusanyaji wa mapato ya halmashauri mbalimbali nchini ni pamoja na sababu kuu mbili.

Ametaja sababu hizo ni kukosekana kwa usimamizi madhubuti wa kuhakikisha kuwa fedha inayokusanywa inahifadhiwa benki pamoja na baadhi ya wasimamizi na wahasibu kukosa uadilifu na kujinufaisha na fedha hiyo.

“Kazi nyingine iliyofanyika ni uchunguzi wa ubadhirifu wa fedha kiasi cha Sh.milioni 861.2 za Chama cha Msingi cha KISANGA Wilaya ya Sikonge mkoani Tabora, ambapo ubadhirifu huo umefanywa na viongozi wa chama hicho wakishirikiana na maafisa ushirika wa Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge. Uchunguzi wa jalada hili umekamilika na watuhumiwa wamefunguliwa kesi Mahakamani.”



Na; Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) imeweka mikakati madhubuti ya kuimarisha mfumo wa usimamizi wa taka kwa kuandaa Mkakati wa Taifa wa usimamizi wa Taka (2025 - 2030) ambao unalenga kupunguza uzalishaji wa taka kwa kutumia dhana ya uchumi rejeshi.

Katika kuhakikisha mnyororo wa usimamizi wa taka unaimarika, Serikali inahamasisha wadau hususan sekta binafsi kuwekeza katika matumizi ya teknolojia za kisasa za kuchakata taka, uwekezaji katika viwanda vya urejelezaji na kuimarisha mifumo ya ukusanyaji wa taka ili kufikia malengo ya kupunguza au kuondoa taka katika Mazingira kwa kuigeuza kuwa malighafi ya uzalishaji wa bidhaa anuwai zinazofaa kwa matumizi mbalimbali.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni ameyasema hayo katika maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Taka Sifuri, Viwanja vya Mnazi Mmoja, jijini Dar es Salaam, Machi 30, 2026.

Amesema Siku ya Kimataifa ya Taka Sifuri huadhimishwa kila mwaka Machi 30 kwa lengo la kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa kupunguza matumizi ya bidhaa zinazopelekea kuzalisha taka, kutumia tena bidhaa kabla ya kugeuzwa taka na kuchakata taka kwa kurejeleza ili kuepuka uchafuzi wa mazingira.

“Kauli mbiu ya kimataifa kwa mwaka huu inatoa hamasa ya "KUWEZESHA TAKA SIFURI KWENYE SEKTA YA CHAKULA" ikiwa na lengo la kuhimiza matumizi endelevu ya vyakula na kupunguza taka zitokanazo na sekta hii. Kwa upande wa Tanzania, kauli mbiu ya Kitaifa inahimiza kutambua "TAKA NI FURSA" ikisisitiza kuwa taka si uchafu bali ni malighafi yenye thamani, endapo itasimamiwa na kuchakatwa vyema.”

“Uzalishaji wa taka umekuwa changamoto kubwa kwa nchi za Ugaibuni na Africa, hususani katika miji mikubwa kama Dar es Salaam, Mwanza na Arusha na takwimu zinaonesha takribani kiasi cha tani zaidi ya millioni 7 za taka ngumu huzalishwa nchini kwa mwaka ambapo wastani wa asilimia 45 hadi 50 tu hukusanywa na kutupwa dampo.

Aidha, amesema asilimia 50 hadi 55 hubaki kwenye mazingira na kuzagaa kwenye mito na mifereji ya maji taka na mitaro ya maji ya mvua. Hata hivyo, matokeo ya Sensa ya Taifa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022 yanaonesha kuwa, asilimia 40 ya kaya zinachoma taka ngumu na asilimia 22 ya kaya zinatumia njia ya ukusanyaji sahihi wa mara kwa mara.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware amesema ni wakati sasa wa kubadili mtazamo kuwa taka si uchafu tu bali ni rasilimali yenye thamani.

Amesema mabaki ya chakula yanaweza kuzalisha mbolea na nishati, plastiki inaweza kurejelezwa na kuwa bidhaa mpya, na chuma chakavu kinaweza kurejelezwa na kuzalisha bidhaa nyingine.

“Ninatoa wito kwa kila mmoja wetu kuanzia maeneo ya makazi, biashara na viwandani kuchukua hatua madhubuti za kupunguza uzalishaji wa taka, kuchambua taka katika vyanzo vyake na kuimarisha utamaduni wa kuchakata taka.”

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mhe. Mhandisi Hamadi Yussuf Masauniakipokea zawadi kutoka kwa Mjumbe wa Bodi Wakurugenzi ya NEMC, Dkt. Abubakar Rajab wakati wa maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Taka Sifuri, Viwanja vya MnaziMmoja, jijini Dar es Salaam, Machi 30, 2026.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mhe. Mhandisi Hamadi Yussuf Masauni(katika), Mkuu wa Wilaya ya Ilala Mhe. Edward Mpogolo na Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware wakiwa katika maadhimisho ya Siku ya Kimataifa yaTaka Sifuri, Viwanja vya Mnazi Mmoja, jijini Dar es Salaam, Machi 30, 2026.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mhe. Mhandisi Hamadi Yussuf Masauniakizungumza na wananchi katika maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Taka Sifuri, Viwanja vya Mnazi Mmoja, jijini Dar es Salaam, Machi 30, 2026.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mhe. Mhandisi Hamadi Yussuf Masauni akizungumza na wananchi katika maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Taka Sifuri, Viwanja vya Mnazi Mmoja, jijini Dar es Salaam, Machi 30, 2026.
Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware akizungumza na wananchi katika maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Taka Sifuri, Viwanja vya Mnazi Mmoja, jijini Dar es Salaam, Machi 30, 2026.
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, amesema kuwa mfumo wa stakabadhi ghalani ni mfumo rasmi wa biashara unaolenga kusimamia mazao yaliyokubaliwa na kuthibitishwa, kwa lengo la kuimarisha masoko na kipato cha wakulima.

Akizungumza Machi 30, 2026, katika kikao cha wadau wa mfumo huo kilichofanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Dodoma, amesema mfumo huo unamruhusu mkulima kuuza mazao yake ghalani na kupata mikopo benki, pamoja na kuuza kwa bei yenye ushindani wa soko la dunia.

Ameeleza kuwa faida za mfumo huo ni pamoja na kuongeza tija, kurahisisha upatikanaji wa masoko ya mazao, pamoja na kuondoa upangaji holela wa bei kwani bei hufuata mwenendo wa soko la kimataifa.

Aidha, amesema mfumo huo unaimarisha uchumi wa wakulima kwa kuwapatia taarifa sahihi za bei na masoko, huku ukiongeza mapato ya serikali kupitia ushuru, kuboresha vipimo sahihi vya mazao na kuimarisha usalama wa chakula nchini.

Amesema serikali imeanzisha mfumo huo ili kuondoa changamoto mbalimbali zikiwemo uuzaji wa mazao kabla ya mavuno, matumizi ya vipimo visivyo rasmi na mifumo kandamizi ya biashara, sambamba na kuboresha ukusanyaji wa mapato ya serikali.

Mkuu wa Mkoa amewapongeza wadau mbalimbali wanaoshiriki katika utekelezaji wa mfumo huo, akiwemo WRRB, TMX, COPRA, DORECU pamoja na Tume ya Ushirika, kwa mchango wao katika kufanikisha mfumo huo mkoani Dodoma.

Ametoa wito kwa DORECU kuanza rasmi utekelezaji wa majukumu yao, kutoa elimu kwa wakulima na kuhamasisha uundwaji wa vyama vya msingi vya ushirika ili kuongeza kasi ya utekelezaji. Pia amesisitiza ujenzi wa maghala zaidi katika maeneo ya kimkakati, akibainisha kuwa hadi sasa maghala 39 tayari yamejengwa.

Vilevile, amesisitiza umuhimu wa kuajiri watumishi wenye weledi katika maghala hayo na kuhakikisha wakulima wanalipwa kwa wakati ili waone matokeo chanya ya juhudi zao.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama Kikuu cha Ushirika Dodoma (DORECU), Theresia Nyoka, amesema mkulima ni mhimili muhimu wa uchumi wa nchi na anapaswa kuheshimiwa. Ameiomba serikali kusaidia vyama vya ushirika kupata mitaji ili viweze kujiendesha kwa ufanisi.

Amesema DORECU imejipanga kuboresha huduma kwa kununua mizani ya kielektroniki 10 na kusambaza kompyuta kwenye vyama vya msingi ili kurahisisha utoaji wa huduma kwa wakulima.

Naye mwakilishi kutoka Wizara ya Kilimo, Aneth Mwangasa, amesema wizara inaendelea kufanya tathmini ya mfumo huo kila baada ya msimu wa kilimo na kutoa kipaumbele kwa mikoa mipya ikiwemo Dodoma, pamoja na kusaidia upatikanaji wa pembejeo kama mbegu na viuatilifu.

Katibu Tawala Msaidizi wa Uchumi na Uzalishaji Mali, Aziza R. Mumba, amesema timu za wilaya zimejipanga kudhibiti usafirishaji haramu wa mazao na kusimamia sheria ndogo ili kuhakikisha mfumo unatekelezwa ipasavyo. Pia amebainisha kuwa ununuzi wa mazao kupitia madalali hautaruhusiwa.

Ametaja mikakati ya mwaka 2026 kuwa ni pamoja na kuhamasisha uzalishaji wa mazao yanayopitia kwenye mfumo, kuandaa na kuboresha maghala, kuimarisha vyama vya ushirika, kuhamasisha usajili wa waendesha maghala, kufanya tafiti na kuboresha miundombinu.

Amesema kuwa Vyama vya ushirika 14 vilitekeleza mfumo wa stakabadhi za ghala na kuuza jumla ya kilo 43,707,331 zikijumhisha ufuta kilo 19,300,802, Mbaazi kilo 24,092,900 na Dengu Kilo 313,629, na Halmashauri zilizofanya minada ya zao la mbaazi ni kondoa Mji, Kondoa, Chemba, Dodoma Jiji na Kongwa.

Mkoa wa Dodoma ni miongoni mwa miongoni mwa Mikoa, inayozalisha mazao ya ufuta, Mbaazi na dengu, ambayo mazao hayo yanauzwa kupitia mfumo wa masoko wa stakabadhi za ghala, na wadau katika utekelezaji wa mfumo huo ni wakulima, mamlaka za serikali za mitaa, vyama vya ushirika, watunza maghala, bodi ya usimamizi wa stakabadhi za ghala, tume ya maendeleo ya ushirka, mamlaka ya udhibiti wa mazao mchanganyiko na soko la bidhaa Tanzania.




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi mbalimbali mara baada ya kupokea Ripoti za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa Mwaka wa Fedha 2024/25, Taarifa ya Mwaka ya Utendaji Kazi wa Taasisi ya Kuzuia na kupambana na Rushwa (TAKUKURU) pamoja na Taarifa ya Mwaka ya Utendaji Kazi ya Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 30 Machi, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye hafla ya kupokea Ripoti za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa Mwaka wa Fedha 2024/25, Taarifa ya Mwaka ya Utendaji Kazi wa Taasisi ya Kuzuia na kupambana na Rushwa (TAKUKURU) pamoja na Taarifa ya Mwaka ya Utendaji Kazi ya Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Ikulu jijini Dar es Salaam, tarehe 30 Machi, 2026.
Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Bw. Charles Kichere akisoma Muhtasri wa Ripoti yake kwa Mwaka wa Fedha 2024/25, Ikulu jijini Dar es Salaam, tarehe 30 Machi, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa Mwaka wa Fedha 2024/25 kutoka kwa Bw. Charles Kichere, Ikulu jijini Dar es Salaam, tarehe 30 Machi, 2026.
Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (TAKUKURU) Bw. Crispin Chalamila akisoma Muhtasari wa Taarifa ya Mwaka ya Utendaji Kazi wa Taasisi hiyo, Ikulu jijini Dar es Salaam, tarehe 30 Machi, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Taarifa ya Mwaka ya Utendaji Kazi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi hiyo, Bw. Crispin Chalamila, Ikulu jijini Dar es Salaam tarehe 30 Machi, 2026.

Mkurugenzi wa Mamlaka ya Kudhibiti Ununuzi wa Umma (PPRA) Bw. Dennis Simba akisoma Muhtasari wa Taarifa ya Mwaka ya Utendaji Kazi wa Taasisi hiyo, Ikulu jijini Dar es Salaam, tarehe 30 Machi, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Taarifa ya Mwaka ya Utendaji Kazi wa Mamlaka ya Kudhibiti Ununuzi wa Umma (PPRA) kutoka kwa Mkurugenzi wa Mamlaka hiyo Bw. Dennis Simba, Ikulu jijini Dar es Salaam, tarehe 30 Machi, 2026.

 


Top News