-Awapongeza Rais Samia, Rais Mwinyi kwa kuendeleza mafanikio


Na Mwandishi Wetu, Zanziba

MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara, Stephen Wasira, amesema kazi iliyofanywa na Muasisi wa mapinduzi na Rais wa Kwanza wa Zanzibar, hayati Sheikh Abeid Amani Karume, ndiyo inayowafanya Wazanzibari watembee kifua mbele kwa haki, uhuru na maendeleo.

Aidha, amewapongeza Rais Dk. Samia Suluhu Hassan na Rais wa Zanzibar na Meenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi kwa kuendeleza malengo ya mapinduzi na kuongoza nchi kwa haki.

Wasira aliyasema hayo hivi karibuni, Mjini Unguja katika kongamano la nane la kumuenzi Hayati Karume lililoandaliwa na Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere.

"Madhumuni ya mapinduzi ya watu wa Zanzibar ni kukomesha upendeleo wa kiuchumi, kijamii na upendeleo wa kisheria, maana uchumi haukuwa kwa Wazanzibari wote, ardhi ilikuwa imechukuliwa na wachache na Wazanzibari watu wazima kazi yao ilikuwa kuangua nazi (wakwezi) kwa wakubwa.

"Mapinduzi yakaleta mabadiliko ambayo yaligawa ardhi ya Zanzibar heka tatu tatu, haki ya uchumi, upendeleo wa sheria kwa maana ya kwamba katika sheria haki unaipata kutegemeana na wewe unatoka wapi hiyo ndio ilikuwa Zanzibar," alisema.

Alisisitiza kumkumbuka hayati Karume, sio kukumbuka miaka yake tangu alipouawa bali ni kukumbuka mazuri aliyoyatenda wakati wa uongozi wake.

"Tunapomkumbuka Karume leo, tunakumbuka mafanikio makubwa ya kuleta umoja wa watu wa Zanzibar. Hivi sasa Zanzibar watu hawabaguliwi kwa misingi hiyo, kazi aliyoianza inaendelea.

"Kwa msingi huo ningependa kutumia nafasi hii kutoa pongezi za dhati kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya Dk. Hussein Ali Mwinyi kwa kuendeleza mawazo hayo ya maendeleo kwa wote," alisema.


HALI ILIVYOKUWA ZANZIBAR

Wasira alisema kongamano hilo shabaha yake ni kutoa elimu kurithisha mambo ya viongozi waliotangulia kwa kizazi kipya.

 "Kama hatusemi na wengine wamezaliwa miaka mingi baadae na hawakuwepo wakati wa mapinduzi wanaweza kudhani hivyo walivyo ndivyo walivyokuwa, lakini ukweli ni kwamba Zanzibar kama ilivyokuwa kwa makoloni mengine katika Afrika hata Zanzibar haki ilikuwa kitu adimu sana kukipata kwa sababu haki ilitolewa kulingana na mahitaji ya rangi ya watu kabila zao, asili yao," alieleza

Kwa mujibu wa Wasira, wakati wa utawala wa Sultan kama mwananchi hakuwa na asili iliyompendeza mtawala hakupewa haki.

 "Kama asili yako haikumpendeza (Sultan) unanyimwa haki, hivyo ndivyo ilivyokuwa. Tunapomkumbuka Hayati Abeid Amani Karume vijana lazima wajue hatukumbuki miaka 54 ya kuuawa kwake, tunakumbuka mchango wake na fikra zake zilizoifikisha Tanzania hapa ilipo, hicho ndicho tunachokumbuka.

Ukikumbuka miaka 54 ya kifo chake hujakumbuka kitu maana hata Afro Shirazi wakati alipouawa walisema wameua kiwiliwili lakini mawazo yamebaki, kwa kauli ya Afro Shirazi mwaka 1972 kilichoondoka ni kiwiliwili cha Karume lakini mawazo yake yanaendelea. Kwa maneno mengine hawakuua mapinduzi waliua mtu.

"Hivyo ndivyo ilivyokuwa Zanzibar kupata haki ni mpaka ujulikane wewe hasa unatokana na kundi lipi...jitihada kubwa za serikali ya Sultan na washirika wake Waingereza ilikuwa kugawa watu, unawagawa halafu unawatawala, unawachonganisha. Hivi ndivyo ilivyokuwa.

"Chama cha Afro Shirazi kitu ambacho walikuwa wanapinga ni kupindisha haki, walikuwa wanataka haki ziende kwa wote bila kujali dini, bila kujali makundi, bila kujali asili ya mtu anakotokea. Hiyo ndio ilikuwa kazi ya Afro Shirazi na ninao ushahidi wa jambo hilo.

Februari 25, 1964 kwa sababu hapakuwa na Bunge hapa, kulikuwa na Baraza la Mapinduzi ndilo lilikuwa linatunga sheria na ndilo lilikuwa linampa mamlaka rais atunge sheria zinazoambatana na sera na Ilani ya Chama cha Afro Shirazi, kwa hiyo tarehe ile Rais alitunga sheria inaitwa DP, na dp ile ilikuwa inasema sheria itakuwa inajulikana kwa jina la usawa, maridhiano na umoja wa watu wa Zanzibar, hiyo ilikuwa mwaka 1964 mwezi mmoja baada ya mapinduzi," alisema.

Wasira alisema Mapinduzi yalileta mabadiliko ambayo yaligawa ardhi ya Zanzibar heka tatu tatu kwa mwananchi.








Mhe. Lazarus Chakwera (kushoto), Rais wa zamani wa Jamhuri ya Malawi na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, Mhe. Shirley Ayorkor Botchwey, amewasili nchini usiku wa tarehe 08 Aprili 2026 usiku kwa ziara ya kikazi. Mhe. Chakwera amepokelewa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Ngwaru Maghembe (kulia).








  • Kupitia toleo hili la nne, Qualcomm inathibitisha tena dhamira yake ya kuimarisha mfumo wa teknolojia ya hali ya juu barani Afrika kupitia ushauri, mafunzo, na mipango ya kukuza miliki bunifu (IP)

 Kampuni ya Qualcomm Incorporated leo imetangaza uteuzi wa kampuni changa au startups 10 kwa mwaka wa nne wa Mpango wa Ushauri wa Qualcomm® Make in Africa. Mpango huu ni sehemu ya Qualcomm Africa Innovation Platform, unaolenga kusaidia maendeleo ya mfumo wa teknolojia ya hali ya juu barani Afrika. Unatoa ushauri na mafunzo, ukiweka mkazo kwenye teknolojia za mawasiliano ya kisasa na uchakataji kama vile Edge AI/ML, kompyuta (compute), IoT (Mtandao wa Vitu), pamoja na jukwaa la maendeleo ya AI (Akili Bandia) la Qualcomm kupitia Arduino.

Mambo Muhimu:

  • Katika fainali ya mpango huu, kampuni changa moja itapata ruzuku kutoka Social Impact Fund ya Qualcomm for Good.

  • Kampuni Changa zote zitapata posho ya dola za Marekani 5,000 baada ya kukamilisha mahitaji ya mpango kwa mafanikio.

  • Qualcomm inatoa rasilimali mbalimbali ikiwa ni pamoja na mwongozo wa kubuni bidhaa kwenye majukwaa ya Arduino AI, ushauri wa biashara, upatikanaji wa wataalamu wa uhandisi, na elimu ya bure ya miliki bunifu kupitia L2Pro Africa.

Kwa toleo la mwaka huu la mpango huu wa kipekee wa ushauri barani Afrika usiohitaji hisa (equity-free), kampuni changa 10 za awali zilichaguliwa kutoka zaidi ya maombi 1,200 kutoka nchi zaidi ya 45 za Afrika. Uchaguzi ulizingatia uwezo wao wa kutumia teknolojia za hali ya juu za mawasiliano na uchakataji katika suluhisho bunifu za mifumo kamili. Sekta zinazowakilishwa ni pamoja na kilimo, teknolojia saidizi, miji janja, miundombinu janja, usafiri wa magari ya umeme (EV), na elimu.

Kampuni Changa za kundi la 2026 ni:

  • Amperra Charging Company (Namibia): Mfumo wa kuchaji magari ya umeme (EV) unaotumia AI (Akili Bandia) na kuendana na gridi ya umeme, kwa ajili ya kukuza matumizi ya EV barani Afrika

  • Anatsor Ltd (Nigeria): Mfumo wa kidijitali wa usimamizi wa ufugaji wa kuku unaoboresha uzalishaji na ufuatiliaji wa afya

  • D-Olivette Labs (Nigeria): Jukwaa la bio-intelligence linalotoa uchambuzi wa data kwa ajili ya kilimo endelevu

  • Mindora Corporation (Zimbabwe): Kibodi ya Braille inayobooresha upatikanaji wa teknolojia kwa watu wenye uoni hafifu

  • MVUTU (Jamhuri ya Kongo): Mfumo wa kuhifadhi mazao kwa baridi unaotumia nishati ya jua na IoT

  • QualiKeeper Investments Ltd (Zambia): Mfumo wa AIoT wa kufuatilia mifugo kwa gharama nafuu maeneo ya vijijini

  • SafeSip (Tanzania): Suluhisho la maji salama linalotumia teknolojia janja kwa maeneo ya mijini na pembezoni mwa miji

  • Sesi Technologies Ltd (Ghana): Kifaa kinachotumia AI kutathmini ubora wa kakao mapema

  • TWave Ltd (Uganda): Mfumo wa kulisha samaki unaotumia nishati ya jua

  • Zerobionic (Kenya): Suluhisho za roboti saidizi kwa watu wenye ulemavu

Ubunifu wa kampuni changa wa mwaka huu unaonyesha ukuaji mkubwa wa mfumo wa ubunifu barani Afrika,” alisema Wassim Chourbaji, Rais wa Mashariki ya Kati na Afrika na Makamu wa Rais Mwandamizi wa Masuala ya Serikali katika Qualcomm. “Kampuni changa hizi zinaonyesha uwezo wa teknolojia kama Edge AI na 5G, na jinsi zinavyoweza kutumika kwa kiwango kikubwa barani Afrika.”

Washiriki watapata majukwaa ya Arduino yenye uwezo wa edge-AI bila malipo, pamoja na ushauri wa kiufundi na biashara. Fabio Violante wa Arduino alisema kuwa vifaa kama Arduino® UNO™ Q vinawawezesha waanzilishi kubadilisha mawazo kuwa mashine janja kwa haraka.

Pia watapata msaada wa maendeleo ya bidhaa na ushauri wa kulinda miliki bunifu, ikiwa ni pamoja na msaada wa usajili wa hataza kupitia Adams & Adams na mafunzo ya IP kupitia L2Pro Africa.

Mwisho wa mpango, kampuni changa zitastahili kupata ufadhili kupitia Qualcomm for Good, pamoja na posho ya dola 5,000 kwa washiriki wote waliokamilisha mpango. Wanaowasilisha haki miliki zao wanaweza kurejeshewa hadi dola 5,000 za gharama za usajili.

Baraza la Umoja wa Mawasiliano Afrika (ATU) linaendelea kuwa mshirika kwa mwaka wa nne mfululizo. Katibu Mkuu John Omo alisema mpango huu unawezesha wabunifu wa Afrika kutumia teknolojia kutatua changamoto za Afrika. 

Kwa maelezo zaidi tembelea:
https://www.qualcomm.com/company/locations/africa/qualcomm-make-in-africa

Kuhusu Qualcomm

Qualcomm ni kampuni inayobuni teknolojia za kompyuta janja na mawasiliano ili kusaidia dunia kukabiliana na changamoto mbalimbali. Kupitia majukwaa yake kama Snapdragon®, inawezesha uzoefu wa kipekee kwa watumiaji na kusaidia biashara kukua kupitia teknolojia za kisasa.

Kuhusu Arduino

Arduino ni jukwaa la wazi la vifaa na programu linalotumika kuunda miradi shirikishi ya teknolojia. Lina watumiaji zaidi ya milioni 33 duniani na linatoa suluhisho kwa IoT, vifaa vinavyovaliwa, uchapishaji wa 3D, na mifumo iliyojengwa ndani (embedded systems).











Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Profesa Palamagamba John Aidan Kabudi kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) kwenye hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 08 Aprili, 2026.Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Festo John Dugange kuwa Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kwenye hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 08 Aprili, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Kwagilwa Reuben Nhamanilo kuwa Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) kwenye hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 08 Aprili, 2026.Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Gerson John Mdemu kuwa Kamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama kwenye hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 08 Aprili, 2026. 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza mara baada ya kuwaapisha Viongozi Wateule, Ikulu ya Chamwino Mkoani Dodoma tarehe 08 Aprili, 2026.
Viongozi mbalimbali wakiwa kwenye hafla ya uapisho ya Viongozi wateule, Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 08 Aprili, 2026.
Viongozi wateule wakiapa Kiapo cha Maadili kwenye hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 08 Aprili, 2026.















Na. MWANDISHI WETU -DODOMA

Watendaji wa Ofisi ya Waziri Mkuu wamekumbushwa kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi, ufanisi na kujituma ili kuhakikisha wanachangia kikamilifu katika kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa 2050, hususan katika maeneo ya sera, uratibu na usimamizi wa utekelezaji wake.

Wito huo umetolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Mhe. Prof. Palamagamba J.A. Kabudi, wakati akizungumza na watumishi wa Ofisi hiyo mara baada ya kuwasili rasmi na kupokelewa na uongozi na watumjshi wa Ofisi hiyo katika Jengo la Ngome Jijini Dodoma tarehe 8 Machi, 2026

Prof. Kabudi alisisitiza umuhimu wa ushirikiano na ubunifu miongoni mwa watumishi ili kuongeza ufanisi wa utendaji kazi.

“Ni muhimu tushirikishane mawazo na kufanya kazi kwa pamoja ili kumsaidia Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kufanikisha adhima ya maendeleo yenye kuleta ustawi na furaha kwa Watanzania," alisema Prof. Kabudi

Aliongezea kuwa upo umuhimu wa kushikamana ili kuendelea kuimarisha utendaji wetu ili kumwezesha Mheshimiwa Waziri Mkuu kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi zaidi.

Aidha, Waziri Kabudi alibainisha kuwa mazingira ya kazi yenye mshikamano na mahusiano ya kifamilia hayapaswi kuwa chanzo cha uzembe au utovu wa nidhamu, bali yawe kichocheo cha kuongeza uwajibikaji na kufikia viwango vya juu vya utendaji.

Katika hatua nyingine, Waziri Kabudi aliwataka watumishi kuendelea kumuombea aliyekuwa Waziri wa Nchi katika Ofisi hiyo, Marehemu William Vangimembe Lukuvi, ili Mwenyezi Mungu amrehemu na kumpa pumziko la milele.

“Nitaendeleza, kadri nitakavyoweza, misingi na jitihada zilizoanzishwa na mtangulizi wangu katika kuijenga Ofisi hii,” aliongeza.

Awali, Naibu Waziri wa Ofisi hiyo, Mhe. Ummy Nderiananga, alimpongeza Prof. Kabudi kwa kuaminiwa na kuteuliwa na Mheshimiwa Rais kushika nafasi hiyo, akiahidi ushirikiano wa dhati kutoka kwa watumishi wote katika utekelezaji wa majukumu yake.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. Jim Yonazi, naye alimpongeza Waziri Kabudi kwa uteuzi huo na kusisitiza kuwa watumishi wako tayari kuongozwa na kushirikiana naye katika kuendelea kuwahudumia wananchi kwa ufanisi.









Na  Diana Byera, Bukoba 

WIZARA ya Katiba na Sheria imeanza kutoa mafunzo kwa wajumbe wa bodi za usuluhishi wa migogoro ya ndoa, kutokana na ongezeko la kesi za talaka nchini, 

Akifungua mafunzo hayo Naibu Katibu Mkuu wa wizara ya Katiba na Sheria  Franklin Rwezimula  amesema mafunzo hayo yameanzia mkoani Kagera kwa  lengo la kuongeza weledi na mbinu mpya za  usuluhishi wa ndoa katika jamii ili kujenga familia bora na jamii yenye mshikamano 

“Takwimu zinaonyesha talaka zilizosajiliwa mwaka 2023 zilikuwa  711,  mwaka 2024  zikapanda hadi 1,569, na  mwaka 2025 talaka  zilizosajiliwa zilikuwa 1,172 na hizo ni zile talaka tu zilitoleawa taarifa na ndoa nyingine zimekuwa zikivunjika kimya kimya  bila kutolewa taaarifa na kuhatarisha   ustawi wa familia na jamii kwa ujumla.”

Amefafanua bodi za usuluhishi zinapaswa kufanya kazi kwa weledi na kujiepusha kuwa mahakimu huku akidai bodi hizo zisiwe sehemu ya kupokea rushwa  Bali zijikite kuondomitafaruku  kutovujisha Siri na Kutenda haki.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Huduma za Sheria kwa umma  Obadia Kamea  amesema uwepo wa wajumbe wa bodi ya usuluhishi Kwa ngazi ya kata nchi nzima unalenga kupunguza Mrundikano wa  kesi za talaka zinazoenda mahakamani  

Amesema pia mafunzo haya yanalenga kuimarisha mbinu mpya , usuluhishi kulingana na hali ya kisasa ya malalamiko  makubwa ya ndoa na migogoro  iliyopo kwa sasa ukilinganisha na miaka ya Zamani .

Awali Issaya Tendega ambaye ni Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Kagera amesema migogoro ya ndoa isipotatuliwa kwa wa wakati inasababisha ofisi za viongozi ngazi ya wilaya na mikoa  kuwa na mrundikano wa kesi ambo ambalo linasababisha viongozi kutumia muda mrefu Kufanya usuluhishi kuliko kufanya kazi Nyingine.

"Ofisi za wakuu wa wilaya na wakuu wa mikoa wanapokea kesi nyingi za ndoa na zinatumia muda mrefu sana ,tunaamini wajumbe wa haya mabaraza wakifanya kazi yao vizuri migogoro ya ndoa itapungua ,tunaomba baada ya mafunzo haya mfaye kazi kwa weledi ili kupunguza kesi nyingi za ndoa mahakamani na ofisi za viongozi"alisema Tendega

Awali Jawadu Mwanandege ambaye ni Mjumbe wa bodi  ya usuhishi wa ndoa ameishukuru Serikali kwa namna inavyoendela kuimarisha mafunzo na mbinu za utatuzi kwa ngazi ya mabaraza ambapo alisema kuwa Mafunzo hayo yatawajengea uwezo wa kufanya usuluhishi na kufanya kazi kwa haki.







Awataka waliopewa dhamana ya usimamizi wazingatie misingi ya utawala bora

 
WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba ameziagiza Mamlaka, Taasisi na Wadau wote waliopewa dhamana ya kusimamia utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025 wabadilike na wahakikishe wanatekeleza wajibu wao kwa kuzingatia misingi ya utawala bora na utawala wa sheria ili kufikia malengo na shabaha zilizoainishwa katika Sera hiyo.

Amesema taarifa za ukaguzi za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali pamoja na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma zinaonesha kuwa changamoto katika ununuzi wa umma siyo Sera, Sheria wala Kanuni, bali ni waliopewa dhamana ya kusimamia Sera, Sheria, Kanuni na Taratibu za Ununuzi.

Waziri Mkuu amesema kuwa sehemu kubwa ya shughuli za ununuzi zinaathiriwa zaidi na mitazamo, hulka na tabia za wataalamu na watendaji ikilinganishwa na upungufu wa masuala ya kisera na kisheria, hivyo amewataka  wadau wa Sekta Binafsi waweke mikakati ya kuimarisha mifumo ya ushirikiano na sekta ya umma ili kunufaika kikamilifu na fursa zilizobainishwa katika Sera hiyo.

Ametoa maagizo hayo leo (Jumatano, Aprili 8, 2026) alipozindua Sera ya Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025 kwa niaba ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, jijini Dodoma. “Leo tunaweka alama muhimu katika historia ya usimamizi wa mali na rasilimali za Taifa letu”.

Amesema hatua hiyo ya kisera inalenga kuchochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi, kuongeza fursa za ajira na kipato, pamoja na kujenga uchumi jumuishi na shindani unaomilikiwa na Watanzania walio wengi. “Kwa ujumla, fursa hizi zinalenga kuchochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi, kuongeza uzalishaji wa bidhaa, Utoaji wa huduma pamoja na kukuza uwiano wa upatikanaji wa bidhaa na huduma”.

“Hii ni kutokana na ukweli kwamba, kwa mara ya kwanza, Tanzania inakuwa na mwongozo mmoja wa kisera unaounganisha na kufungamanisha mtazamo wa kimfumo na hatua zote muhimu katika mnyororo wa ugavi, kuanzia ununuzi, ugomboaji, upokeaji, urejeshaji, uhifadhi, matumizi, usambazaji hadi uondoshaji wa mali za umma”.

Waziri Mkuu amesema Sera hiyo inaweka mkazo katika matumizi ya malighafi na wataalamu wa ndani, kukuza viwanda vya ndani, kuimarisha miundombinu ya kiteknolojia, pamoja na kuzingatia hifadhi ya mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. “Kwa kufanya hivyo, mnyororo wa ugavi umeimarishwa na kuwa chombo cha kimkakati cha kuongeza uzalishaji na ugavi wa bidhaa na huduma pamoja na uendelevu na ushindani wa Taifa katika Masoko ya kikanda na kimataifa”.

Wakati huo huo, Waziri Mkuu amezitaka Wizara, Idara zinazojitegemea, Wakala za Serikali, Taasisi na Mashirika ya Umma, Ofisi za Wakuu wa Mikoa, Mamlaka za Serikali za Mitaa na Wadau wa Sekta Binafsi watekeleze Sera hiyo kwa Weledi, Uwazi na Uwajibikaji.

Amesema kufikiwa kwa malengo na shabaha za Sera hiyo kutategemea zaidi dhamira, fikra, mtazamo, uwazi, ushirikishwaji na uwajibikaji wa wadau wote katika ngazi zote za usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi.

Pia, Waziri Mkuu amezisisitiza Mamlaka zote zinazohusika zihakikishe kuwa utekelezaji wa Sera hii unaimarisha ushiriki wa wazalishaji wa ndani, wafanyabiashara wadogo na wa kati, pamoja na makundi maalumu ya kijamii ili kufikia malengo jumuishi na usawa miongoni mwa washiriki.

Amesema Wizara na Taasisi zote za umma zinapaswa kufanya Mapitio ya Sera, Sheria, Kanuni na Miongozo mbalimbali inayokinzana na misingi ya Sera hii ili kuwa na mazingira rafiki katika usimamizi wa shughuli za Mnyororo wa Ugavi.

Hafla hiyo imehudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - Fedha na Mipango, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Dkt. Juma Malik Akil, Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Profesa Elisante Ole Gabriel ambaye amemuwakilisha Jaji Mkuu wa Tanzania, Jaji Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti, Mashimba Ndaki aliyemuwakilisha Spika wa Bunge, Wakuu wa Mkoa, Makatibu Tawala wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa Halmashauri, Makatibu Tawala wa Wilaya.





 

Na Sixmund Begashe, Dodoma

Wananchi wa Jimbo la Kasulu Vijijini wameendelea kunufaika na uwepo wa mwekezaji katika kitalu cha Makere Forest Reserve kwa kupata mgao wa fedha za maendeleo ya jamii zaidi ya  Shilingi Milioni 12 kila mwaka kinacholipwa na mwekezaji kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya vijiji.

Hayo yamesemwa Bungeni Jijini Dodoma na Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji, alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Jimbo hilo Mhe. Edibil Kazala Kinyoma alipotaka kujua "Je, ni kwa kiasi gani wananchi wa Jimbo la Kasulu Vijijini wananufaika na uwepo wa Mwekezaji wa kitalu cha Makere Forest Reserve".

Dkt. Kijaji amesema kuwa kwa kuzingatia vipaumbele vya vijiji husika katika Mwaka wa Fedha 2024/2025 Vijiji vya Kagera Nkanda, Chekenya na Kabulanzwili vililipwa Shilingi 4,356,435.67 kila kimoja. 

"Vilevile, mgao wa fedha zinazotokana na asilimia 25 ya ada ya wanyamapori wanaowindwa katika kitalu husika kwa mujibu wa Kifungu cha 137 cha Sheria ya Fedha ya Mwaka 2025 zinalipwa na Serikali kwa Halmashauri husika".  Alifafanua Dkt. Kijaji

Ameongeza kuwa asilimia 60 ya fedha hizo hutumika kutekeleza miradi ya maendeleo na asilimia 40 shughuli za uhifadhi katika vijiji vinavyozunguka kitalu husika.

 "Sambamba na manufaa yaliyotajwa, katika kipindi cha mwaka 2024/25 na 2025/26 mwekezaji kwa kushirikiana na Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) wamechangia miradi ya jamii yenye thamani ya shilingi 166,475,000". Aliongeza Dkt. Kijaji 

Aidha, Dkt. Kijaji amesema kuwa fedha hizo zimetumika kufadhili kambi ya huduma ya matibabu ya macho katika Halmashauri ya Kasulu, madawati 100 katika Shule za Msingi Chekenya (25), Nyakasanda (25) na Nyantuku (50) na uchimbaji wa visima vya maji sita (6) katika Shule za Msingi Kamganza, Kasasa, Mwitiri, Chekenya na Nyantuki pamoja na Kituo cha Afya cha Kagerankanda.



 


Top News