Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mhe. Dkt. Rhimo Nyansaho, amewapongeza viongozi wa  Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kwa juhudi wanazozifanya za kuimarisha ulinzi na usalama nchini.

Amesema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari kwenye maadhimisho ya miaka 50 ya biashara ya kimataifa jijini Dar es Salaam  Sabasaba, Julai 6, 2026, amesisitiza kuwa vyombo hivyo vya ulinzi vimekuwa vikiendelea kulinda amani ya nchi, jambo linalowezesha wananchi kufanya shughuli za maendeleo na kufanikisha utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya 2050.

Aidha amesema shirika  la JKT linafanya kazi za uzalishaji mali pamoja na kuwafundisha vijana, hatua inayosaidia kuwaandaa kujitegemea na kujiajiri.

Ameeleza kuwa kupitia maonesho hayo, taasisi hizo zimepata nafasi ya kuonesha shughuli mbalimbali zinazofanyika kwenye vikosi vyao, ikiwemo kutoa huduma kwa wananchi na mafunzo kwa vijana.

Amesema kampuni ya usafi na unyunyuzi dawa ya SUMA JKT ambayo imefanikiwa kuajiri vijana 4,800, hatua inayoonesha mchango wa taasisi hizo katika kupunguza changamoto ya ajira nchini.



Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Ubongo (MOI) imesema itaendelea kuimarisha tafiti zinazolenga kuzalisha afua za matibabu zinazozingatia mazingira na vinasaba vya Watanzania, ili kuboresha huduma za matibabu ya magonjwa ya mifupa na mfumo wa fahamu.

Akizungumza na waandishi wa habari Mkurugenzi Mtendaji wa MOI, Balozi Dkt. Mpoki Ulisubisya, Jijini Dar es Salaam Julai 6, 2026, kwenye Maadhimisho ya Miaka 50 ya Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba).

Amesema mara nyingi tiba zinazotumika hutokana na matokeo ya tafiti zilizofanyika katika nchi zilizoendelea pamoja na baadhi ya nchi za bara la Afrika, ambapo afua hizo zinaweza kuwa zimezingatia watu wenye vinasaba tofauti, hivyo wao wameona umuhimu wa kufanya tafiti zitakazozalisha afua zinazokidhi mazingira ya Tanzania.

Aidha, amesema MOI imetimiza miaka 30 tangu kuanzishwa kwake na imeendelea kujikita katika maeneo makuu matatu ambayo ni kutoa huduma kwa wagonjwa wa mifumo ya ubongo na mifupa, kufundisha huduma hizo kwa wananchi na wataalam katika ngazi ya shahada ya kwanza, shahada ya pili na ubobezi, pamoja na kufanya tafiti.

Pia amesema taasisi hiyo imeweza kutoa mafunzo kwa wananchi na wataalam kutoka ndani na nje ya Tanzania, hususan katika ukanda wa Afrika Mashariki, Kati, Kusini na Magharibi, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha huduma za afya katika kanda hiyo.





📍Dar es Salaam

Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Dkt. Janet Lekashingo, amesema Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 imeipa sekta ya madini nafasi ya kimkakati ya kuongoza mageuzi ya uchumi wa Tanzania kupitia uongezaji thamani wa madini, ushirikishwaji wa watanzania na matumizi ya teknolojia za kisasa katika shughuli za uchimbaji wa madini.

Akizungumza mapema leo Julai 6, 2026, alipotembelea mabanda ya taasisi zilizo chini ya Wizara ya Madini katika Kijiji cha Madini kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), Dkt. Lekashingo amesema Tume ya Madini imejipanga kikamilifu kutekeleza malengo ya Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 ili sekta ya madini iwe nguzo muhimu ya ukuaji wa uchumi na maendeleo endelevu.

Amesema utekelezaji wa dira hiyo unalenga kuongeza thamani ya madini ndani ya nchi badala ya kuyasafirisha ghafi, kuimarisha utafiti wa jiolojia ili kubaini maeneo mapya yenye rasilimali za madini, kuongeza ushiriki wa watanzania katika miradi ya uchimbaji wa madini pamoja na kuhamasisha matumizi ya teknolojia rafiki kwa mazingira na zinazoongeza usalama migodini.

Aidha, amewataka wananchi kutembelea banda la Tume ya Madini ili kupata elimu kuhusu huduma zinazotolewa na Tume pamoja na fursa zilizopo katika mnyororo wa thamani wa madini, ikiwemo taratibu za kushiriki biashara ya madini na kuuza madini kupitia masoko na vituo vya ununuzi wa madini.

Katika hatua nyingine, Dkt. Lekashingo amewapongeza viongozi na watumishi wa Tume ya Madini kwa kuvuka lengo la ukusanyaji wa mapato katika mwaka wa fedha 2025/2026, akisema mafanikio hayo yanadhihirisha uwajibikaji na usimamizi madhubuti wa sekta ya madini.

“Mmetuheshimisha kwa kuvuka lengo la ukusanyaji wa mapato, lakini tusibweteke. Bado tuna wajibu mkubwa wa kuhakikisha tunavuka lengo la kukusanya shilingi trilioni 1.4 katika mwaka wa fedha 2026/2027,” amesema.

Wakati huohuo, Dkt. Lekashingo ametembelea mabanda mbalimbali ya taasisi zilizo chini ya Wizara ya Madini, ikiwemo Tume ya Madini, Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST), Kituo cha Jemolojia Tanzania (TGC) na Wadau wa Madini kabla ya kutembelea mabanda ya Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Banda la Zanzibar na Wizara ya Nishati.

Akiwa katika banda la Wizara ya Nishati, Dkt. Lekashingo ameiomba Wizara hiyo kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kuhakikisha umeme unafikishwa katika maeneo yote yenye shughuli za uchimbaji na uchenjuaji wa madini nchini ili kuongeza tija kwa wachimbaji, kuimarisha uzalishaji, kuongeza thamani ya madini na kuendeleza mchango wa sekta ya madini katika ukuaji wa uchumi na Pato la Taifa.











 



-Asema kasi ya maendeleo chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, amani, uchumi, afya, maji na miundombinu vimemshawishi kubadili msimamo wa kisiasa.

Na Oscar Assenga,TANGA

Baada ya zaidi ya miaka 30 ya kuwa mwanasiasa wa upinzani, aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Wilaya ya Tanga, Rashid Jumbe, amefanya uamuzi mkubwa wa kisiasa kwa kujiunga na Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Jumbe, ambaye kwa muda mrefu alikuwa mmoja wa viongozi mashuhuri wa Chadema mkoani Tanga, amesema uamuzi wake umetokana na kuridhishwa na utekelezaji wa miradi ya maendeleo pamoja na juhudi za Serikali ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha amani, umoja na ustawi wa wananchi.

Akizungumza wakati wa hafla ya kumpokea ndani ya CCM iliyoongozwa na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga, Rajab Abdurhaman, Jumbe alisema hakufanya uamuzi huo kwa papara, bali baada ya kutafakari kwa kina na kujiridhisha kuhusu mwelekeo wa maendeleo ya taifa.

"Nilikuwa mpinzani kwa zaidi ya miaka 30, lakini leo nimeamua kuhitimisha safari hiyo. Kilichonishawishi zaidi ni kazi kubwa inayofanywa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan katika kuwaletea Watanzania maendeleo na kuhakikisha amani ya nchi inalindwa," alisema.

Alieleza kuwa pia amevutiwa na utekelezaji wa falsafa ya 4R inayosisitiza maridhiano, ustahimilivu, mageuzi na kujenga upya, akisema imeongeza mshikamano na kuimarisha mazingira ya maendeleo nchini.



Akizungumzia Mkoa wa Tanga, Jumbe alisema mabadiliko yanayoonekana katika sekta mbalimbali ni ushahidi wa dhamira ya Serikali ya kuufungua mkoa huo kiuchumi.

Alitaja kuongezeka kwa shughuli katika Bandari ya Tanga, ujenzi wa bandari kavu pamoja na utekelezaji wa miradi mingine ya kimkakati kuwa miongoni mwa hatua zilizochochea ukuaji wa uchumi na kuongeza fursa za biashara.


"Nimekuwa nikipaza sauti kwa miaka mingi nikitaka Tanga ifunguliwe kiuchumi. Leo naona hilo limefanyika. Mizigo imeongezeka bandarini, bandari kavu zimejengwa na shughuli za biashara zinaendelea kukua," alisema.

Katika sekta ya afya, Jumbe alisema maboresho yaliyofanyika katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga Bombo, upatikanaji wa dawa na vifaa tiba pamoja na ujenzi wa zahanati katika kata na mitaa mbalimbali vimempa imani kuwa Serikali inaendelea kuboresha huduma kwa wananchi.

Aidha, alisema upanuzi wa huduma za maji na umeme pamoja na utekelezaji wa mpango wa Bima ya Afya kwa Wote ni miongoni mwa hatua zinazoonyesha dhamira ya Serikali ya kuinua maisha ya Watanzania.

"Nilijiuliza ni hoja gani itanifanya nibaki upinzani wakati maendeleo yanaonekana wazi. Tanga ina amani, huduma zinaimarika na wananchi wanaendelea kunufaika na miradi ya maendeleo," alisema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga, Rajab Abdurhaman, alisema chama hicho kinaendelea kuimarisha umoja na mshikamano ili kuongeza uwezo wake wa kusimamia maendeleo na kuwatumikia wananchi.



Alisema tangu alipopewa dhamana ya kuongoza CCM mkoani humo, ameweka mkakati wa kuimarisha chama kupitia ushirikiano na wanachama pamoja na kuwakaribisha viongozi kutoka vyama vingine vya siasa.

Rajab alisema mkakati huo umeendelea kuzaa matunda, akieleza kuwa kujiunga kwa Rashid Jumbe ni ishara ya kuongezeka kwa imani ya baadhi ya viongozi wa upinzani kwa juhudi za maendeleo zinazotekelezwa na Serikali.

"Jumbe alikuwa mmoja wa viongozi wakubwa wa upinzani katika Wilaya ya Tanga. Tuliahidi kwamba tutamshawishi aje kushirikiana nasi katika kujenga chama na kuwaletea wananchi maendeleo, na leo tumefanikiwa," alisema.</



Na Janeth Raphael MichuziTv 

Serikali imewataka wanachama wa vyama vya ushirika nchini kuwa mstari wa mbele katika kulinda amani ya Tanzania kwa kuchagua viongozi waadilifu, kushiriki kikamilifu katika shughuli za vyama vyao na kusimamia rasilimali za ushirika kwa uwajibikaji ili kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Wito huo umetolewa na Naibu Waziri wa Kilimo,  David Silinde (Mb), aliyemwakilisha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Ushirika Duniani yaliyofanyika Julai 6, 2026, jijini Dodoma.

Akifunga maadhimisho hayo yaliyobeba kaulimbiu ya "Ushirika kwa Dunia Yenye Amani," Mhe. Silinde alisema ushirika una nafasi kubwa katika kujenga mshikamano wa jamii na kudumisha utulivu wa nchi, akisisitiza kuwa maendeleo ya vyama vya ushirika hayawezi kupatikana bila kuwepo kwa mazingira ya amani na utulivu.

Amesema kila mwanaushirika ana wajibu wa kuwa mlinzi wa amani kwa kuhakikisha anashiriki katika uchaguzi wa viongozi waadilifu, kushiriki vikao vya vyama vyao na kutoa mchango katika maamuzi yanayolenga kuviimarisha vyama hivyo.

"Ushirika hustawi katika mazingira ya amani, mshikamano na ushirikiano. Hivyo, kila mwanaushirika ana jukumu la kulinda tunu hiyo muhimu kwa maendeleo ya Taifa," alisema Mhe. Silinde.

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri huyo alitoa onyo kali kwa watu wanaojihusisha na ubadhirifu wa mali za vyama vya ushirika, akisisitiza kuwa Serikali haitamvumilia mtu yeyote atakayebainika kutumia vibaya mali za wanachama au kukiuka sheria za usimamizi wa vyama vya ushirika.

Aidha, amewataka wanachama kuwa na utamaduni wa kushiriki kikamilifu katika shughuli za vyama vyao, akieleza kuwa ushiriki wa wanachama ndiyo msingi wa kujenga vyama vyenye nguvu, uwajibikaji na uwezo wa kuchangia maendeleo ya wananchi na Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake, Msajili na Mtendaji Mkuu wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC), Dkt. Benson Ndiege, alisema sekta ya ushirika inaendelea kupiga hatua kubwa kutokana na maboresho mbalimbali yanayofanywa na Serikali, hususan matumizi ya mifumo ya kidijitali katika uendeshaji wa vyama vya ushirika.

Amesema matumizi ya teknolojia yameongeza uwazi, ufanisi, uadilifu na uwajibikaji katika usimamizi wa shughuli za ushirika, sambamba na kuhakikisha sheria, kanuni na misingi ya utawala bora inazingatiwa.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Tanzania Federation of Cooperatives (TFC),  Tito Haule, alisema mchango wa sekta ya ushirika katika uchumi wa Taifa unaendelea kuongezeka kwa kasi, huku akibainisha kuwa mauzo ya mazao kupitia vyama vya ushirika yamefikia thamani ya shilingi trilioni nne.

Amesema mafanikio hayo yanaonesha nafasi muhimu ya ushirika katika kuwawezesha wakulima na kuchochea ukuaji wa uchumi wa nchi, huku akitoa wito kwa wanachama kuendelea kuimarisha ushirikiano na kusimamia vyama vyao kwa uwajibikaji ili kuongeza tija na manufaa kwa wanachama pamoja na Taifa.

Maadhimisho ya Siku ya Ushirika Duniani mwaka 2026 yamehitimishwa kwa msisitizo wa kuendelea kuimarisha ushirika kama chombo muhimu cha kujenga uchumi shirikishi, kulinda amani na kuharakisha maendeleo endelevu nchini.











WAZIRI MKUU Dkt Mwigulu Nchemba amewaalika wafanyabiashara kutoka Ufaransa wawekeze nchini Tanzania kwani ina fursa ya kutengeneza ajira, kuhamisha ujuzi na kujenga uchumi wa viwanda kwa faida ya nchi zote mbili.

“Leo tumefanya mjadala wa kibiashara na sote tumeshuhudia makubaliano yakisainiwa baina ya Tanzania Private Sector Foundation na International Chamber of Commerce (ICC). Makubaliano haya siyo tu mkataba wa kawaida bali ni daraja la kutupeleka kwenye mafanikio makubwa huko mbele,” amesema.

Waziri Mkuu ametoa wito huo leo (Jumatatu, Julai 6, 2026) wakati akizungumza na washiriki wa mjadala wa kibiashara baina ya Tanzania na Ufaransa (Tanzania-France Business Roundtable) uliofanyika kwenye ofisi za ubalozi wa Tanzania jijini Paris, Ufaransa.

“Kwa hiyo ninawahimiza wafanyabiashara wa Ufaransa mtumie vyema fursa hii ya kipekee. Maamuzi yatakayofanywa leo ndiyo yatakayoamua mwelekeo wa sekta za uchumi za kesho kwa nchi zetu. Wale watakaowekeza nchini Tanzania hivi sasa, hawatakuwa tu sehemu ya mageuzi ya uchumi wetu, bali watakuwa washirika wa thamani katika kujenga moja ya uchumi wenye ushindani mkubwa zaidi barani Afrika kwa vizazi vijavyo.”

Dkt. Mwigulu amesema Ufaransa inao utaalamu wa hali ya juu na wa kiwango cha kimataifa katika teknolojia, uhandisi, nishati, miundombinu, viwanda, masuala ya fedha, na huduma za afya.

“Kwa upande wake, Tanzania inao utulivu wa kisiasa, nafasi yake ya kijiografia imekaa kimkakati, inazo rasilimali nyingi za asili, fursa shindani za uwekezaji, usimamizi thabiti wa uchumi pamoja na nguvukazi ya vijana wengi na yenye ari kubwa barani Afrika.”

Amesema maeneo hayo yana nguvu na yanakamilishana kwani katika umoja wake yanajenga fursa za kipekee za kukuza maendeleo endelevu na ustawi wenye manufaa ya pande zote mbili.

“Tunapoanza kwa ujasiri kutekeleza malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Serikali yetu itaendelea kuwa thabiti katika kuhakikisha kunakuwepo mazingira yanayotabirika, yenye uwazi na rafiki kwa biashara, ambapo uwekezaji unalindwa, ushirikiano unathaminiwa, na mafanikio yanawanufaisha wadau wote,” amesisitiza.

Waziri Mkuu pia alishuhudia utiaji saini wa Hati ya Makubaliano (MoU) kati ya Chama cha Kimataifa cha Biashara cha Ufanransa (ICC) na Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), ambapo Mtendaji Mkuu wa TPSF, Bw. Deo Massawe alibadilishana hati hiyo na Naibu Katibu Mkuu wa ICC, Bw. Julian Kassum.

Mapema, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo, aliwaeleza washiriki wa mjadala huo kwamba kitendo kilichofanyika leo kinaendana na malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ambayo inasisitiza ushiriki wa sekta binafsi kwa asilimia 70 katika kuchochea maendeleo ya uchumi.

Kwa upande wake, Rais wa TPSF, Bi. Angelina Ngalula alisema Tanzania ipo katika nafasi ya kipekee ya kuwa kitovu cha mageuzi ya uchumi barani Afrika chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

“Kwa miaka mingi, Ufaransa imekuwa mshirika muhimu wa Tanzania katika uwekezaji. Hata hivyo, kwa sasa tunapaswa kuelekeza nguvu zetu katika kujenga ushirikiano wa muda mrefu utakaokuza uhamishaji wa teknolojia, kukuza sekta ya utalii, huduma za kifedha pamoja na uchumi wa kidijitali. TPSF iko tayari kuwezesha ushirikiano huo kati ya wafanyabiashara wa Tanzania na wenzao wa Ufaransa,” alisema.

Baadhi ya kampuni za Ufaransa zilizoshiriki mjadala huo zinajihusisha na usimamizi wa nishati ya jua (ikiwemo mifumo ya taa za barabarani), usafirishaji, maji, nishati, ujenzi, viwanda, mazingira na ufugaji wa viumbe maji (ikiwemo uzalishaji wa mwani wa baharini). Kampuni nyingine ni waendeshaji wa huduma za satelaiti wanaotoa suluhisho bunifu kwa huduma za utangazaji wa sauti na picha, intaneti ya kasi (broadband), huduma za data, usafiri wa baharini na anga. Aidha, kulikuwa na wazalishaji wa mabomba maalumu yanayotumika katika sekta ya mafuta na gesi.

Mkutano huo pia ulihudhuriwa na Waziri wa Madini, Anthony Mavunde; Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi; Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa na Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika UNESCO, Balozi Saidi Othman Yakubu; Mtendaji Mkuu wa MEDEF International, Bw. Philippe Gautier; Rais wa Baraza la Biashara la Ufaransa na Afrika Mashariki, Bi. Celine Gouveia; pamoja na wajumbe kutoka sekta binafsi ya Tanzania na ujumbe wa wafanyabiashara kutoka Ufaransa.









Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Bw. Yusuph Juma Mwenda, amesema Mamlaka hiyo itaendelea kutekeleza maelekezo ya Rais kuhusu kuimarisha ulipaji wa kodi kwa hiari kwa kuhakikisha kodi inasimamiwa na kukusanywa kwa haki na weledi ili kujenga imani ya walipakodi kwa TRA.

Akizungumza katika kikao cha tathmini ya utendaji kazi wa TRA kwa mwaka wa fedha 2025/2026, Kamishna Mkuu Mwenda amesema katika kikao hicho pia watajadili na kuweka mikakati ya namna ya kutekeleza maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyoyatoa wakati wa maadhimisho ya miaka 30 ya TRA na utoaji wa Tuzo za Rais Julai Mosi mwaka huu.

Mwenda amesema TRA itaendelea kuwaheshimu walipa kodi wote, huku ikichukua hatua stahiki dhidi ya wanaokwepa kulipa kodi kwa mujibu wa sheria na kuwarudisha kwenye mstari kwa heshima.

Amesisitiza pia kuwa hakutakuwa na "kodi ya dhuluma", akieleza kuwa walipa kodi hawapaswi kuidhulumu nchi kwa kukwepa kodi, na kwa upande mwingine TRA haitawadhulumu walipakodi kupitia makadirio yasiyo sahihi ya kodi.

Aidha, amesema ili kuongeza ulipaji wa kodi kwa hiari ni lazima kujenga imani ya walipa kodi kwa kuhakikisha usimamizi wa kodi wa haki, matumizi yenye uwajibikaji ya mapato ya kodi pamoja na kuboresha huduma zinazotolewa na TRA ili kuwezesha biashara na kurahisisha ulipaji wa kodi.

Mwenda amesema ushirikiano kati ya TRA na walipa kodi umewezesha mafanikio makubwa ya ukusanyaji wa mapato katika kipindi cha miaka 30 ya mamlaka hiyo.

Amebainisha kuwa makusanyo ya kodi yameongezeka kutoka takribani shilingi trilioni 21 kwa mwaka wakati Rais alipoingia madarakani hadi kufikia shilingi trilioni 37.96, sawa na ukuaji wa zaidi ya asilimia 77.
















Top News