Na Mwandishi Wetu

MTAALAM katika Sekta ya Mafuta nchini Dkt Sajad Habib Rai amempongeza Makamu wa Rais Ndejembi kwa kuapishwa kwake kushika nafasi hiyo huku akisisitiza hana shaka na uwezo na uadilifu wake katika kulitumikia Taifa la Tanzania akimsaidia Rais Samia Suluhu Hassan

Akizungumza jijini Dar es Salaam siku moja baada ya uapisho wa Makamu Rais huyo Ikulu ya Cha Chamwino, Dodoma, Dkt Sajad amesema ana imani kubwa na Kiongozi huyo huku akimpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa uteuzi wa Ndejembi.

Dkt Sajad ambaye ni Meneja Mkazi wa Mansoor Industries nchini, amesema hana shaka na uwezo wa Ndejembi katika uongozi akisisitiza kwa sifa na uwezo alionao ni msaada tosha katika usaidizi kwa Dkt Samia Suluhu Hassan.

" Kwa kipindi kifupi alichohudumu katika Wizara ya Nishati kwa nafasi ya Uwaziri , Mheshimiwa Ndejembi amekuwa mtu muhimu aliyesimama kikamilifu katika kuahughulikia masuala mbalimbali, hii ni sifa ambayo siyo kila Kiongozi anayo" amesema Dkt Sajad

Amesema hatua ya Rais Samia Hassan kumteua na baadae jina lake kupitishwa na Bunge, kunatokana uwezo wake hatua iliyomfanya kiongozi huyo Mkuu wa nchi kujenga imani dhidi yake hivyo anapaswa kuendelea kumuonesha imani hiyo wakati huu anapomsaidia katika majukumu makubwa zaidi Kiongozi.

Mtaalamu huyo wa Nishati pamoja na Mawasiliano aliyeisaidia Serikali katika 'upigaji mafuta' bandarini kupitia ubunifu wake wa mfumo maalumu wa udhibiti wa mafuta (BIL) amewataka wananchi kumuamini Ndejembi sambamba na kumpa ushirikiano wakati huu anapotekeleza wajibu wake.

Pamoja na wananchi Dkt Sajad pia amewataka watendaji wote wa Serikali, Wabunge pamoja na wafanyabiashara nchini wakiwemo waliomo katika sekta ya mafuta kuendelea kumuunga mkono Makamu wa Rais Ndejembi ili aweze kutimiza kikamilifu majukumu yake ya kumsaidia Rais Samia na Taifa kwa ujumla.

Ndejembi ambaye amehudumu katika nafasi mbalimbali za utumishi pamoja na uongozi ikiwemo ya Waziri wa Utumishi baadae Waziri wa Nishati ameapishwa jana kushika nafasi hiyo ya Makamu wa Rais baada ya mtangulizi wake Dkt Emmanuel Nchimbi kujiuzuru hivi karibuni.



Na Mwandishi Wetu
SERIKALI imezitaka shule nchini kuweka kipaumbele kwenye mafunzo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kwa wanafunzi wao ili kwenda sanjari na dunia ya sasa ya utandawazi na teknolojia inayokua kwa kasi. Imesema teknolojia inakwenda kwa kasi kubwa hivyo shule zinapaswa kuwa na miundombinu bora ya wanafunzi kujifunza TEHAMA, huku ikiipongeza shule ya Bunazi Green Acres iliyoko mji mdogo wa Bunazi, Kata ya Kassambya, wilayani Missenyi, kwa kuwa mfano kwenye eneo la mafunzo ya TEHAMA.

Ushauri huo ulitolewa mwishoni mwa wiki na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Missenyi mkoani Kagera, Phocus Rwegasira, wakati wa mahafali ya 10 ya shule hiyo yaliyofanyika shuleni hapo, ambapo alikuwa mgeni rasmi. Alisisitiza kuwa mafunzo ya teknolojia ni muhimu kwani dunia inakwenda kwa kasi kwenye eneo hilo, huku akisisitiza pia umuhimu wa ushirikiano kati ya wazazi, walimu na jamii katika kuhakikisha watoto wanapata elimu bora na malezi yanayowaandaa kuwa viongozi na wataalamu wa baadaye.

Alisema pamoja na shule hiyo kuweka miundombinu bora na ya kisasa, mafanikio ya mwanafunzi hayawezi kutenganishwa na juhudi za walimu, wazazi na uongozi wa shule, hivyo kila upande unapaswa kutekeleza wajibu wake kwa umakini. Rwegasira pia aliwahimiza wahitimu kuwa na nidhamu, bidii na kujituma katika masomo yao ya ngazi zinazofuata, akiwataka kutumia fursa za elimu kujenga maisha yao na kuchangia maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.

Aidha, aliwataka wazazi kuendelea kuwa karibu na watoto wao, kufuatilia maendeleo yao ya kitaaluma na kuwajengea misingi mizuri ya maadili. Katika hafla hiyo, Rwegasira alikabidhi vyeti kwa baadhi ya wahitimu, huku akipongeza uongozi wa Bunazi Green Acres kwa kutimiza miaka 10 ya mahafali na kuendelea kutoa mchango katika sekta ya elimu nchini.

Mkurugenzi wa Shule ya Bunazi Green Acres, Jackline Rushaigo, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya shule, wazazi na jamii katika kuhakikisha wanafunzi wanapata elimu bora na malezi yenye misingi ya maadili. Alisema mafanikio yaliyofikiwa na shule hiyo ni matokeo ya juhudi za pamoja za walimu, wazazi, wanafunzi na wadau wa elimu, huku akiwapongeza wanafunzi waliohitimu kwa hatua waliyofikia na kuwataka kuendelea kuwa na nidhamu, bidii na kujituma katika masomo yao ya ngazi zinazofuata.

Aidha, aliwashukuru wazazi na walezi kwa kuendelea kuiamini shule hiyo na kushirikiana na uongozi katika kuhakikisha wanafunzi wanapata mazingira bora ya kujifunza na kukua kitaaluma na kimaadili.

Mkuu wa shule hiyo, Geoffrey Moses, alisema shule hiyo tangu kuanzishwa kwake miaka 10 iliyopita imepata mafanikio makubwa kwani wanafunzi wake wote wamekuwa wakipata daraja A katika matokeo ya mitihani ya kitaifa inayotangazwa na Baraza la Taifa la Mitihani (NECTA). Alisema shule imejitahidi kuboresha miundombinu yake kwa kujenga majengo sita ya madarasa yenye vyumba 25 vya kujifunzia na imejenga maabara ya kisasa ya TEHAMA yenye huduma za mtandao kwa ajili ya mafunzo kwa vitendo.

Alisema shule imejitahidi kujenga maktaba yenye vitabu vingi vya kiada na vya ziada na mabweni sita yenye vitanda kwa kila mwanafunzi, na kwamba mazingira hayo ndiyo yameiwezesha shule kutoa huduma bora na matokeo mazuri kila mwaka. “Tunajivunia kwamba miaka yote 10 tangu shule ianze tumefanya vizuri kitaaluma, tumeshatoa wanafunzi 500 kwa miaka yote 10 na muda wote huo shule imekuwa ikipata wastani wa alama 251 ambayo ni daraja A bora,” alisema.

Aidha, alisema mafanikio ya shule hiyo yametokana na juhudi kubwa za walimu wake, nidhamu ya wanafunzi na ushirikiano mkubwa wa wazazi na serikali kuanzia ngazi ya kata hadi ngazi ya Wizara. “Mwaka huu tuna wahitimu 64 wa darasa la saba ambao tunaamini wataendeleza historia yetu nzuri ya kitaaluma kwa sababu wameandaliwa vizuri sana,” alisema.

Aidha, Mkuu huyo wa shule alisema katika kutambua ulimwengu unavyokwenda kwa kasi kwenye teknolojia, shule imeanzisha maabara ya TEHAMA yenye mtandao ili kuwapa wanafunzi ujuzi wa kompyuta kwa vitendo. “Wanafunzi wetu wanajivunia kutumia teknolojia kwa kujiamini na kwa ubunifu, hivyo tunaamini ujuzi huu utawaandaa kushindana na kufanikiwa katika dunia ya sasa,” alisema mwalimu Moses.



Mkuu  wa Wilaya ya Chato, Mhe. Louis Peter Bura, akikabidhi vifaa kinga vilivyogharamiwa na Serikali kwa mafundi wa uchomeleaji vyuma na useremala katika Kijiji cha Kalebezo, Kata ya Nyamirembe Wilaya ya Chato. Mafundi hao walipatiwa mafunzo ya usalama na afya kazini na OSHA na kisha kukabidhiwa vifaa hivyo ambavyo ni pamoja na kofia ngumu, glovu, barakoa na makoti ya usalama.
Mkuu wa Wilaya ya Chato, Mhe. Louis Peter Bura akifungua mafunzo ya usalama na afya mahali pa kazi yaliyotolewa na OSHA kwa kikundi cha mafundi wanaojihusisha na uchomeleaji vyuma na useremala katika Kijiji cha Kalebezo, Kata ya Nyamirembe, Wilaya ya Chato Mkoani Geita.
Mwanakikundi cha Smart Welders and Funirtures, kilichopo Kijiji cha Kalebezo, Kata ya Nyamirembe, Wilaya Chato, akionesha mfano wa matumizi sahihi ya vifaa kinga katika shughuli za uchomeleaji vyuma baada ya kushiriki mafunzo ya usalama na afya kazini yaliyotolewa na Taasisi ya OSHA kwa wanakikundi tajwa.
Meneja wa OSHA Kanda ya Ziwa, Lodgard Bishanga, akiwasilisha mada katika mafunzo ya kuwajengea uelewa wa vihatarishi vya kiusalama na afya mafundi wa uchomeleaji vyuma na useremala katika Kijiji cha Kalebezo, Kata ya Nyamirembe Wilaya ya Chato.

Na Mwandishi Wetu
MKUU wa Wilaya ya Chato, Mhe. Louis Peter Bura, amesema kasi kubwa ya ukuaji wa uchumi katika Mkoa wa Geita imepelekea uhitaji wa huduma za usalama na afya mahali pa kazi kuongezeka ambapo ameutaka Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) kuhakikisha upatikanaji wa huduma za ukaguzi na ushauri wa masuala ya usalama na afya katika maeneo ya kazi nchini.

Ametoa kauli hiyo wakati akifungua mafunzo ya usalama na afya mahali pa kazi yaliyotolewa na OSHA kwa kikundi cha mafundi wanaojihusisha na uchomeleaji vyuma na useremala katika Kijiji cha Kalebezo, Kata ya Nyamirembe, Wilaya ya Chato Mkoani Geita.

Mafunzo hayo ambayo ni sehemu ya utekelezaji mpango mkakati wa Taasisi ya OSHA yametolewa kwa watu 15 ambao ni wanakikundi cha Smart Welders and Funirtures ambao kituo chao kimekuwa kikitumika kutoa mafunzo ya ufundi kwa wananchi wa Kata ya Nyamirembe na maeneo ya karibu.

Mkuu wa Wilaya huyo amesema kwa kipindi cha miaka mitatu tangu mwaka 2024, Wilaya ya Chato imeshuhudia ongezeko kubwa la shughuli za kiuchumi zikiwemo shughuli za uchimbaji madini.

“Kipekee niwashukuru sana OSHA kwa kuendelea kutekeleza ipasavyo jukumu lenu la msingi la kusimamia usalama na afya katika maeneo ya kazi nchini. Lakini naomba niwakumbushe kwamba maeneo mengi yanayokuwa kiuchumi yanahitaji sana huduma zenu ambapo Mkoa wa Geita hususan Wilaya ya Chato ni miongoni mwa maeneo hayo,” ameeleza Mheshimiwa Bura na kuongeza:“Hivyo, niwaombe kuangalia maeneo haya kwa jicho la pekee kwani huko nyuma mlikuwa hamjulikani lakini kwasasa watu wanawatambua umuhimu wenu na wanahitaji huduma zenu za ukaguzi wa mifumo ya usalama na afya, uchunguzi wa afya za wafanyakazi, mafunzo na ushauri wa kitaalam juu ya uboreshaji wa mazingira ya kazi.”

Aidha, DC Bura amewapongeza OSHA kwakutoa mafunzo na msaada wa vifaa kinga kwa kikundi cha mafundi ambao shughuli zao zinagusa maisha ya maelfu ya wakazi wa Wilaya ya Chato.

Ameahidi kuendelea kushirikiana na OSHA katika kuhamasisha wakazi wa Chato kuzingatia kanuni bora.

Meneja wa OSHA Kanda ya Ziwa, Lodgard Bishanga, amesema mafunzo husika usalama na afya katika shughuli mbalimbali za kiuchumi zinazotekelezwa katika Wilaya hiyo huku akiwataka wamiliki wa maeneo ya kazi kuwapa ushirikiano wataalam wa OSHA.

Amesema lengo la kuwajengea uelewa wa vihatarishi vya kiusalama na afya katika shughuli zao za ufundi pamoja na mbinu za kudhibiti vihatarishi husika.

“Sambamba na kupatiwa mafunzo, washiriki wamekabidhiwa vifaa kinga vya mfano yakiwemo makoti ya usalama, glovu, kofia ngumu na barakoa ambavyo vimegharamiwa na serikali kama sehemu ya kuendelea kuhamasisha uzingatiaji wa kanuni bora za usalama na afya katika shughuli za uzalishaji

Kwa upande wao washiriki wa mafunzo hayo wakiwemo Lulinda Makoye Manyema naNeema Kalebo wameishukuru Serikali kwakuwajengea uelewa wa masuala ya usalama na afya kazini pamoja na kuwapatia vifaa kinga.

“Tumejifunza mambo mengi sana kupitia mafunzo haya ikiwemo jinsi ya kukuza na kulinda usalama tunapokuwa katika karakana zetu ikiwemo kuwa na mpangilio mzuri wa mashine na vifaa.

Aidha, tumejifunza jinsi ya kutoa huduma ya kwanza endapo itatokea ajali katika shughuli zetu za kila siku,” ameeleza Neema Kalebo, mshiriki wa mafunzo.

Wanakikundi cha Smart Welders and Funirtures, kilichopo Kijiji cha Kalebezo, Kata ya Nyamirembe, Wilaya Chato, wakiwa katika picha ya pamoja na Meneja wa Kanda ya Ziwa wa OSHA, Lodgard Bishanga (wakwanza kushoto) na Afisa Maendeleo Nyamirembe, Sarah Seizure Hamza (wakwanza kulia) baada ya kushiriki mafunzo ya usalama na afya kazini yaliyotolewa na Taasisi ya OSHA kwa wanakikundi tajwa.

KWAKO Mama yangu mpendwa, Dkt. Samia Suluhu Hassan, Assalaam aleykum warahmatullah wabarakatuh!, Shikamoo Mama!

Natumai hujambo Mama yangu, na unaendelea vema na majukumu yako mazito ya kuliongoza na kulijenga Taifa letu la Tanzania. Najua dhamana uliyonayo si ndogo, na najua kila siku mbele yako inakuja na majukumu, matarajio na wakati mwingine changamoto zinazohitaji hekima, uvumilivu na moyo wa ziada.

Mama Rais Samia, waswahili wanasema, “barua ni nusu ya kuonana.” Nami nimeona nikutumie barua hii ya wazi, nikitumaini maudhui yake uyapokee kama vile unavyomuona mwanao anayeketi mbele yako na kukuambia yaliyo moyoni mwake. Siandiki kwa nia ya kukufundisha uongozi, kwa sababu najua dhamana uliyonayo na uzoefu unaokufanya uwe ulipo leo. Naandika kwa sababu mimi ni Mtanzania ninayependa kuona nchi yangu ikiendelea kusonga mbele.

Mama Rais Samia, nimetafakari sana yote yaliyotokea, yanayoendelea kutokea na hata yale tunayodhani yanaweza kutokea huko mbele. Nimetafakari kuhusu taifa letu, kuhusu uongozi wako, kuhusu changamoto zinazojitokeza na kuhusu matarajio makubwa waliyonayo Watanzania. Ghafla, nikajikuta nimekaa mezani, kalamu ikiwa mkononi, nikaanza kukuandikia barua hii ya wazi.

Mama Rais Samia, huenda barua hii isiwe na muhuri wa Serikali, isiwe na nembo ya taasisi yoyote na wala isiwe na cheo chochote nyuma ya jina langu. Lakini ina kitu kimoja muhimu: ina moyo wa Mtanzania anayekuandikia kiongozi wake kwa heshima, kwa nia njema na kwa matumaini kwamba ujumbe huu utakufikia.

Mama Rais Samia, najua kipindi hiki si rahisi. Najua katika safari ya uongozi kuna nyakati ambazo mambo huenda kama ulivyopanga, lakini pia kuna nyakati ambazo matukio huja ghafla na kulazimisha kiongozi kutafakari upya hatua zinazofuata. Ndiyo maana nimeona nikufikishie ujumbe huu mmoja muhimu: Usikate tamaa, Mama. Endelea kujenga nchi yetu.

Rais wangu Dkt. Samia, katika siasa na uongozi, kuondoka kwa mtu mmoja hakupaswi kuwa sababu ya safari ya taifa kusimama. Watu huja na kuondoka, nafasi hubadilika na nyakati hubadilika, lakini nchi hubaki. Tanzania bado ipo, Watanzania bado wana matumaini na mbele yako bado kuna kazi kubwa ya kulijenga taifa hili.

Rais wangu Dkt. Samia, si kila hatua ya uongozi huwa nyepesi. Kuna nyakati ambazo kiongozi hukutana na changamoto zisizotarajiwa, mabadiliko ya kisiasa na maamuzi ya watu aliokuwa akifanya nao kazi kwa karibu. Hayo ni sehemu ya safari ya uongozi, na katika nyakati kama hizi, kinachohitajika zaidi ni utulivu wa akili, hekima na uwezo wa kuangalia mbele.

Rais wangu Dkt. Samia, tunafahamu kwamba kipindi hiki si cha kawaida baada ya Makamu wako Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi, kutangaza kujiuzulu nafasi hiyo. Lakini tukio hilo lisikufanye uone kama safari ya Serikali yako imepata mwisho. Badala yake, lichukulie kama sehemu ya changamoto za uongozi na sababu ya kuongeza nguvu katika kusimamia majukumu uliyopewa na Watanzania.

Rais wangu Dkt. Samia, usife moyo. Usiruhusu changamoto za kisiasa zikupunguzie kasi ya kazi ya kulijenga taifa. Endelea kuwa mtulivu, sikiliza sauti mbalimbali, tafakari kwa kina na chukua maamuzi yenye maslahi mapana ya Tanzania. Wakati mwingine, uimara wa kiongozi hauonekani wakati mambo yako sawa; huonekana zaidi pale anapokutana na mawimbi.

Rais wangu Dkt. Samia, una dhamana kubwa mbele ya Watanzania. Ulipoomba ridhaa yao katika uchaguzi mkuu wa Oktoba, 2025, uliwaahidi mambo mbalimbali kuhusu mustakabali wa nchi yao. Sasa wananchi wanataka kuona ahadi hizo zikigeuka kuwa matokeo. Kazi iliyopo mbele yako si kuangalia sana nani ameondoka au nani amebaki, bali kuhakikisha Tanzania inaendelea kusonga mbele.

Rais wangu Dkt. Samia, ongeza juhudi katika uchumi, ajira, elimu, afya, kilimo, miundombinu na uwekezaji. Lakini zaidi ya yote, endelea kuangalia maisha ya Mtanzania wa kawaida anayehangaika kutafuta chakula, mzazi anayesubiri huduma bora za afya kwa familia yake, kijana anayehitaji ajira na mfanyabiashara anayehitaji mazingira rafiki ya kufanya biashara.

Rais wangu Dkt. Samia, endelea kusikiliza wananchi. Nguvu kubwa ya Serikali haipo katika ofisi kubwa wala magari ya misafara; ipo katika uwezo wa kusikia kilio cha wananchi na kukifanya kuwa sehemu ya ajenda ya Serikali kama ufanyavyo wewe. Wananchi wanahitaji kuona kwamba uongozi wao unawasikia, unawajali na unafanya kazi kwa ajili yao.

Rais wangu Dkt. Samia, Tanzania ni kubwa kuliko mtu mmoja, nafasi moja au tukio moja la kisiasa. Serikali ina taasisi, ina mifumo na ina watendaji. Kwa hiyo, mabadiliko katika nafasi moja yasiruhusiwe kuvuruga mwelekeo wa taifa. Kazi ya Serikali lazima iendelee, miradi iendelee, uchumi uendelee na huduma kwa wananchi ziendelee kuboreshwa.

Rais wangu Dkt. Samia, uongozi hupimwa zaidi wakati wa changamoto kuliko wakati mambo yanapokuwa rahisi. Hiki kinaweza kuwa kipindi kigumu, lakini pia kinaweza kuwa nafasi muhimu kwako kuonyesha zaidi uwezo wako wa kiuongozi, uvumilivu, hekima na weledi katika kuliongoza taifa letu.

Rais wangu Dkt. Samia, Watanzania wanahitaji amani, utulivu na mazingira yatakayowawezesha kufanya kazi na kujenga maisha yao. Wanahitaji kuona tofauti za kisiasa hazigeuki kuwa kikwazo cha maendeleo. Wanahitaji kuona taasisi za Serikali zikifanya kazi kwa ufanisi na viongozi wakitumia madaraka yao kwa ajili ya maslahi ya wananchi.

Rais wangu Dkt. Samia, usikubali changamoto ya leo ikufanye usahau wajibu wa kesho. Historia ya uongozi haijengwi kwa namna kiongozi anavyokabiliana na siku nzuri pekee, bali pia kwa namna anavyosimama imara wakati wa misukosuko na kuhakikisha taifa halianguki.

Rais wangu Dkt. Samia, endelea na kazi. Jenga Tanzania. Timiza yale uliyowaahidi Watanzania. Ongeza maarifa, hekima, juhudi na weledi. Wakati huu unahitaji uongozi unaotazama mbele, unaotanguliza taifa na unaojua kwamba dhamana uliyonayo ni kubwa kuliko changamoto yoyote ya kisiasa inayoweza kujitokeza.

Rais wangu Dkt. Samia, changamoto zitapita, watu watabadilika na nyakati zitabadilika, lakini Tanzania itaendelea kubaki. Kinachohitajika sasa ni uongozi wenye utulivu, hekima, uadilifu, uwajibikaji na maono ya mbali.

Rais wangu Dkt. Samia, huu ndiyo wakati wa kuangalia mbele zaidi kuliko nyuma. Huu ndiyo wakati wa kuimarisha timu yako, kusimamia kwa karibu utekelezaji wa mipango ya Serikali na kuhakikisha kila ahadi iliyotolewa kwa wananchi inapata majibu katika vitendo.

Rais wangu Dkt. Samia, ujumbe wangu kwako ni mmoja tu: Usikate tamaa. Jenga nchi. Endelea kufanya kazi kwa ajili ya Watanzania. Tanzania inahitaji uongozi unaotazama mbele.


Ni mimi mwanao Rashid Mtagaluka

Mbagala, Dar es Salaam

28/08/2026

Simu: 0718 406 242


WALIMU 328 kutoka shule 10 za Sekondari katika Jiji la Tanga wanapigwa msasa kupitia semina maalumu inayolenga kuwaongezea ujuzi na mbinu za ufundishaji, hatua inayolenga kuongeza ufaulu wa wanafunzi wa Kidato cha Pili na Nne.
Semina hiyo inaendeshwa na Taasisi ya Tanzania Centre For Education kupitia mradi wa Tanga Yetu, unaofadhiliwa na Foundation Botnar na kutekelezwa kwa kushirikiana na Innovex, ikiwa ni sehemu ya kampeni ya kukuza ufaulu katika shule za Jiji la Tanga.


Akizungumza wakati wa semina hiyo iliyofanyika katika Shule ya Sekondari Nguvumali, Mkurugenzi Mtendaji wa Tanzania Centre for Education Yusuf Ogutu alisema mafunzo hayo ni mwendelezo wa semina zilizolenga kuwajengea uwezo walimu katika masomo mbalimbali.
Alisema katika hatua hiyo walimu wa masomo ya Historia, Jiografia, Business Studies na Bookkeeping wamepatiwa mafunzo, huku awali semina ikiwa imefanyika katika Shule ya Sekondari Kihere kwa walimu wa Civics, Kiswahili, Kiingereza, Historia ya Tanzania na Maadili.

Ogutu alisema mpango huo unalenga kuhakikisha walimu wanakuwa na uelewa na lugha moja katika kukabiliana na changamoto zinazowakabili wanafunzi na hatimaye kuboresha ufaulu.

“Tunawapatia walimu maarifa na mafunzo, pamoja na kuwawezesha gharama za usafiri kutoka walikotoka na kurejea. Hii ni sehemu ya mpango mpana wa kuhakikisha kampeni ya kukuza ufaulu katika Jiji la Tanga inafikia malengo,” alisema.
Alisema kampeni hiyo inatekelezwa kwa hatua mbalimbali, ambapo awamu ya kwanza iliwahusisha wanafunzi, hatua ya pili ni walimu na awamu inayofuata itawahusisha waratibu wa elimu ngazi ya kata, maafisa elimu wa wilaya pamoja na kamati za malezi na wazazi.

Kwa mujibu wa Ogutu, mpango huo unalenga kuwafanya wadau hao kuwa na uelewa unaofanana katika kuhakikisha wanashirikiana kutafuta suluhisho la changamoto zinazoathiri ufaulu wa wanafunzi.

Alisema hadi sasa walimu 85 tayari wamefikiwa kupitia mafunzo hayo, huku idadi hiyo ikitarajiwa kuongezeka hadi kufikia walimu 100 katika awamu inayoendelea, kabla ya kukamilishwa kwa mafunzo ya walimu wa masomo ya sayansi.
Ogutu alisema jumla ya walimu 328 katika shule 10 wanatarajiwa kunufaika na mpango huo, ambao unalenga kutoa mchango katika kuboresha matokeo ya wanafunzi wa Jiji la Tanga.

Wakufunzi kutoka shule bora
Aidha, alisema walimu wanaopatiwa mafunzo hayo wanafundishwa na wakufunzi wenye uzoefu kutoka baadhi ya shule zilizofanya vizuri kitaifa, hatua inayolenga kuwapatia mbinu bora za ufundishaji.

Alizitaja baadhi ya shule hizo kuwa ni Mzumbe, Marian Boys na Feza Boys, ambazo zimekuwa zikifanya vizuri katika mitihani ya kitaifa.
Alisema pia kuna wakufunzi kutoka Canossa pamoja na shule mbalimbali za Serikali zilizowahi kufanya vizuri kitaifa.

“Tunawaamini sana walimu kwa sababu wao ndiyo injini ya matokeo. Ukiwapiga msasa walimu na kuwaongezea uwezo, unakuwa umeweka msingi mzuri wa kuboresha ufaulu wa wanafunzi,” alisema.
Alisema katika semina hizo walimu wanapata nafasi ya kujadili changamoto mbalimbali za ufundishaji, ikiwemo mada ambazo zimekuwa zikiwasumbua, ili kupata ufumbuzi na kuhakikisha wanakuwa na uelewa unaofanana katika ufundishaji.

Alisema kupitia mpango huo, matarajio ni kuona walimu wakiboresha namna ya kufundisha na wanafunzi wakipata uelewa mzuri wa masomo, jambo litakalosaidia kuongeza ufaulu katika mitihani ya Kidato cha Pili na Nne.
Mpango huo ni sehemu ya juhudi za Tanga Yetu za kuwaunganisha wanafunzi, walimu, wazazi na wadau wengine wa elimu katika kutafuta njia za kuboresha kiwango cha ufaulu katika shule za Jiji la Tanga.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amewasili leo, tarehe 30 Agosti 2026, jijini Belgrade, Jamhuri ya Serbia, kumwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Mkutano Maalum wa Ngazi ya Juu wa Kumbukumbu ya Miaka 65 tangu kufanyika kwa Mkutano wa Kwanza wa Wakuu wa Nchi wa Harakati za Nchi Zisizofungamana na Upande Wowote (NAM).

Rais Dkt. Mwinyi amewasili akiwa ameambatana na ujumbe wake, akiwemo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo, pamoja na viongozi wengine wa Serikali.

Katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Nikola Tesla, Rais Dkt. Mwinyi amepokelewa na Naibu Waziri Mkuu ambaye pia ni Waziri wa Uchumi wa Jamhuri ya Serbia, Mhe. Adrijana Mesarović, pamoja na Balozi wa Tanzania nchini Italia ambaye pia anaiwakilisha Tanzania katika Jamhuri ya Serbia, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk.







Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali itaendelea kushirikiana kwa karibu taasisi za dini likiwemo kanisa Katoliki katika kuimarisha huduma za kijamii, maendeleo na ustawi wa wananchi, akisisitiza kuwa mchango wa taasisi za dini ni sehemu muhimu ya safari ya maendeleo ya Tanzania.

Dkt. Mwigulu ameyasema hayo leo Jumapili, Agosti 30, 2026, katika maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 25 ya Jimbo Katoliki la Mpanda, yaliyofanyika mkoani Katavi, ambapo amesema Serikali inatambua mchango wa Kanisa Katoliki katika maendeleo ya nchi, hususan katika sekta za elimu, afya na huduma za kiroho.

“Serikali inatambua mchango wa Kanisa na baba Askofu. Kila tunapotaja maendeleo ya nchi yetu, kuanzia mwanzo mpaka hapa tulipofika, hatuwezi kuyataja kwa kina maendeleo hayo bila kutaja mchango wa Kanisa.”

Amesema ushirikiano kati ya Serikali na Kanisa umeendelea kuwa muhimu katika kuhakikisha huduma za kijamii na shughuli za maendeleo zinaimarika, akisisitiza kuwa milango ya Serikali itaendelea kuwa wazi kwa Kanisa na taasisi nyingine za dini katika masuala yanayolenga ustawi wa wananchi.

“Niwahakikishie Serikali itaendelea kushirikiana na Kanisa na popote pale mlipo na jambo msisite, milango yetu iko wazi ili tuweze kuhakikisha kwamba tufanye jambo lolote linalotufurahisha.”

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ametoa maelekezo kwa viongozi wa Mkoa wa Katavi na mamlaka husika kuharakisha utekelezaji wa miradi ya barabara, maji na umeme, akisisitiza kuwa wananchi wanapaswa kupata huduma hizo kwa wakati.

Amesema maandalizi ya kukabiliana na uwezekano wa kutokea kwa El Niño yanapaswa kwenda sambamba na hatua za vitendo, ikiwemo ujenzi na uboreshaji wa mifereji na madaraja ili kupunguza athari za mafuriko.

Kuhusu huduma za maji, Waziri Mkuu ameitaka Wizara ya Maji na wahusika wa mradi wa maji Mpanda kuhakikisha wananchi wanapata huduma hiyo ifikapo Desemba 2026, huku akisisitiza pia kuharakishwa kwa miradi ya barabara inayounganisha Katavi na mikoa jirani.

Aidha, Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea kuchukua hatua za kuboresha mazingira ya haki kwa wananchi, akitangaza kuwa Serikali inaelekea kufuta sheria inayohusu utaifishaji wa mifugo, akieleza kuwa hatua hiyo inalenga kuondoa changamoto za wananchi kunyang’anywa mifugo yao.

“Katika Bunge hili linaloendelea tunakwenda kufuta sheria ya utaifishaji wa mifugo... kumekuwepo na majeraha makubwa ya watu kunyang’anywa katika baadhi ya maeneo. Tunataka tuondoe hayo ili kuhakikisha kwamba wananchi wetu wanaepukana na hayo.”

Pia ametoa maelekezo kwa wasimamizi wa sheria kuacha kukamata vitendea kazi vya wananchi kama pikipiki, bajaji na magari katika utekelezaji wa sheria za makosa mbalimbali, akisisitiza umuhimu wa kutumia utaratibu wa kisheria wa adhabu na faini.

Kwa upande wake, Askofu wa Jimbo Katoliki la Mpanda, Mhashamu Baba Askofu Eusebius Nzigilwa, amemshukuru Waziri Mkuu kwa kutenga muda na kushiriki katika maadhimisho hayo, akisema uwepo wake umeonesha heshima na kuthaminiwa kwa Jimbo la Mpanda na Kanisa Katoliki Tanzania.

“Ninakushukuru sana. Tunaona hiyo ni heshima kwa Jimbo letu na kwa Kanisa Katoliki Tanzania, na hivyo tunaomba Mwenyezi Mungu azidi kuwaongoza na kuwajalia neema na hekima katika kutuongoza sisi raia na wananchi wenu.”

Naye Balozi wa Baba Mtakatifu nchini Tanzania anayemaliza muda wake, Mhashamu Askofu Mkuu Angelo Accattino, amesisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano kati ya Serikali na Kanisa Katoliki, akisema ushiriki wa viongozi wa Serikali na viongozi wa dini mbalimbali katika maadhimisho hayo ni ishara ya mahusiano mema kwa ajili ya ustawi wa jamii.

Maadhimisho hayo yamefanyika katika kuadhimisha miaka 25 tangu kuanzishwa kwa Jimbo Katoliki la Mpanda mwaka 2001, huku viongozi wa Kanisa wakieleza kuwa katika kipindi hicho Jimbo limepiga hatua katika huduma za kichungaji, elimu, afya na ujenzi wa miundombinu kwa ajili ya jamii.

Waziri Mkuu amewapongeza viongozi wa Kanisa, waamini na wananchi wa Jimbo Katoliki la Mpanda kwa kufanikisha Jubilee hiyo, akiwataka kuendelea kushirikiana na Serikali katika kujenga jamii yenye amani, mshikamano na maendeleo.





























Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) uko kwenye mchakato wa kufanya marekebisho ya Sheria ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, Sura ya 395, kwa lengo la kupanua wigo wa wanachama, kuendana na mahitaji ya sasa ya huduma za afya na kuimarisha uendelevu wa Mfuko.

Marekebisho hayo pia yanalenga kuimarisha udhibiti wa matumizi mabaya ya Mfuko, ikiwemo udanganyifu unaoweza kufanywa na baadhi ya wanachama, waajiri na watoa huduma za afya lakini kwenda sambamba na sheria Mama ya Bima ya Afya kwa Wote.

Akizungumza katika ukumbi wa mikutano wa NHIF, Kinondoni, Dar es Salaam, wakati wa kupokea maoni ya wadau kuhusu mapendekezo ya marekebisho ya sheria hiyo, Meneja wa Huduma za Sheria wa NHIF, Matamus Fungo, amesema sheria hiyo iliyotungwa mwaka 1999 inahitaji maboresho ili iendane na mabadiliko yaliyopo katika sekta ya afya na mwelekeo wa utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote.

“Tunataka sheria yetu iweze kuboreshwa ili iwezeshe watu wengi zaidi kujiunga na pia kuziba mianya ya matumizi mabaya ya kadi yanayofanywa na baadhi ya wanachama wasio waaminifu” amesema.

Amesema marekebisho hayo yanatarajiwa kuongeza idadi ya wanachama, kuimarisha uendelevu wa Mfuko na kuweka mifumo madhubuti zaidi ya kudhibiti udanganyifu na matumizi yasiyofaa ya huduma za bima ya afya.

Kuzingatia Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote

Kwa upande wake, Wakili wa Serikali kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Mwenda Tulalemwa, amesema marekebisho ya sheria yanapaswa kuzingatia mahitaji ya makundi mbalimbali ya wananchi pamoja na kuendana na Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote, ili kuhakikisha hakuna mgongano wa kisheria.

Amesema wadau waliotoa maoni wamependekeza maboresho katika maeneo mbalimbali, ikiwemo mfumo wa malipo kwa vituo vya kutolea huduma za afya, huduma kwa watu wasio na uwezo na watu wenye ulemavu.

Aidha, miongoni mwa mapendekezo yaliyotolewa ni kuongeza umri wa watoto wanaotambuliwa kama wategemezi kutoka miaka 21 hadi 25, hatua inayolenga kuendana na mahitaji ya familia na mazingira ya sasa.

Naye Wakili wa Mahakama Kuu na mwanachama wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Ferdinand Makole, amesema marekebisho ya sheria yanaweza kuwa fursa muhimu ya kuongeza urahisi, ufanisi na ubora wa huduma zinazotolewa na NHIF.

Amesema sheria inapaswa kuweka mazingira yatakayowezesha Mfuko kutoa huduma zinazokidhi mahitaji ya wanachama na wananchi kwa ujumla, huku ikizingatia uendelevu wa Mfuko.

Kwa upande wake, Mwanasheria wa Bohari ya Dawa (MSD), Brighton Mtigani, amesema ushirikishwaji wa wananchi na wadau mbalimbali ni muhimu katika kuhakikisha sheria inayoandaliwa inaendana na mahitaji yanayobadilika ya jamii.

Amesema ushirikishwaji huo utasaidia kujenga mfumo unaozingatia usawa katika upatikanaji wa huduma za afya na kuhakikisha makundi mbalimbali yanapata huduma bila vikwazo visivyokuwa vya lazima.

Maoni ya wadau kuchangia maboresho ya rasimu

Naye Ofisa Sheria Mwandamizi kutoka Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania, Japhes Daudi, amesema maoni yaliyotolewa na wadau yamechukuliwa na yataendelea kutumika katika kuboresha rasimu ya mapendekezo ya marekebisho ya Sheria ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya.

Kwa ujumla, mchakato huo unalenga kuhakikisha Sheria ya NHIF inaendana na mazingira ya sasa ya utoaji wa huduma za afya na mwelekeo wa Serikali wa kuhakikisha wananchi wanapata huduma za afya kupitia mfumo wa Bima ya Afya kwa Wote.

Marekebisho hayo yanatarajiwa kupanua wigo wa wananchi wanaoweza kunufaika na bima ya afya, kuimarisha udhibiti wa matumizi ya Mfuko, kuboresha huduma kwa wanachama na kuimarisha uendelevu wa NHIF, sambamba na kuchangia utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote nchini.




Top News