Fedha hizo zitasaidia utekelezaji wa maeneo matatu muhimu ya kijamii ambayo ni kupunguza vifo vya akina mama na watoto wakati wa kujifungua, kugharamia upasuaji wa watoto wenye matatizo ya moyo, pamoja na kuimarisha huduma za upandikizaji wa uloto kwa watoto wanaoishi na ugonjwa wa selimundu (Sickle Cell).
Mbio hizo, ambazo zimeendelea kujijengea hadhi kama moja ya matukio makubwa zaidi ya michezo nchini, zilihusisha washiriki kutoka Tanzania na mataifa mbalimbali, huku zikishuhudia ushindani mkubwa kati ya wanariadha wa Tanzania na Kenya katika mbio za kilomita 21 na 42. Dkt. Nchemba, pamoja na viongozi mbalimbali wa Serikali, taasisi na sekta binafsi, walishiriki mbio za kilomita tano (5) kuhamasisha mazoezi na maisha yenye afya.
Akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi zawadi kwa washindi na wadau wa mbio hizo, Dkt. Nchemba alisema mafanikio ya NBC Dodoma Marathon yanaonesha jinsi ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi unavyoweza kuleta matokeo yenye manufaa makubwa kwa jamii.
Alisema ongezeko la washiriki kutoka 1,500 mwaka 2020 hadi zaidi ya 13,000 mwaka 2026 ni ushahidi wa mwamko mkubwa wa Watanzania katika kushiriki michezo, kuzingatia afya zao na kuunga mkono shughuli za maendeleo kupitia michezo.
"NBC Dodoma Marathon imekuwa zaidi ya mashindano ya riadha. Leo ni jukwaa linalounganisha Watanzania na marafiki kutoka mataifa mbalimbali kwa lengo la kufanya jambo kubwa zaidi—kuokoa maisha. Nawahimiza Watanzania kujenga utamaduni wa kufanya mazoezi mara kwa mara ili kujikinga dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza kama vile kisukari, shinikizo la damu, magonjwa ya moyo na figo," alisema Dkt. Nchemba.
Aidha alisema Serikali itaendelea kuboresha miundombinu ya barabara katika Jiji la Dodoma kwa kupanua na kuboresha barabara muhimu, hatua itakayorahisisha shughuli za usafirishaji na wakati huo huo kuongeza usalama wa washiriki wa mbio hizo katika miaka ijayo.
Waziri Mkuu pia aliutaka uongozi wa Mkoa wa Dodoma kuendelea kuziunga mkono mbio hizo kutokana na mchango wake mkubwa katika kukuza uchumi wa jiji hilo kupitia ongezeko la wageni, shughuli za utalii wa ndani, biashara za hoteli, migahawa, usafiri na huduma nyingine zinazochochewa na tukio hilo.
Awali, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Bi. Rosemary Senyamule, alisema NBC Dodoma Marathon imeendelea kuwa kichocheo muhimu cha uchumi wa mkoa huo kwa kuongeza mzunguko wa fedha na kutoa fursa kwa wafanyabiashara wadogo na wakubwa kila mwaka.
Aliishukuru Benki ya NBC kwa kuendelea kuwa mshirika mkubwa wa maendeleo ya Mkoa wa Dodoma kupitia uwekezaji wake katika afya, michezo na maendeleo ya jamii.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC, Bw. Theobald Sabi, alisema mafanikio ya mbio hizo yanaakisi dhamira ya benki hiyo ya kuendelea kutumia biashara kama chachu ya kuleta maendeleo ya kijamii.
Alisema kati ya fedha zilizokusanywa, shilingi milioni 600 zimeelekezwa moja kwa moja katika utekelezaji wa malengo makuu ya NBC Dodoma Marathon kupitia taasisi tatu zinazotoa huduma muhimu za afya nchini.
Katika hafla hiyo, Dkt. Nchemba na Bw. Sabi walikabidhi hundi za misaada ambapo: Shilingi milioni 200 zilikabidhiwa Taasisi ya Benjamin Mkapa kwa ajili ya kupanua programu ya ufadhili wa wakunga ili kuboresha huduma za afya ya uzazi, Shilingi milioni 200 zilikabidhiwa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) kwa ajili ya kugharamia upasuaji wa watoto wenye matatizo ya moyo na Shilingi milioni 200 zilikabidhiwa Hospitali ya Benjamin Mkapa kusaidia huduma za upandikizaji wa uloto kwa watoto wenye ugonjwa wa selimundu.
"Mafanikio haya yanatokana na dhamira yetu ya kuhakikisha mafanikio ya biashara yanaenda sambamba na ustawi wa jamii. Tunawashukuru washiriki wote, wadhamini na wadau mbalimbali waliochangia kufanikisha NBC Dodoma Marathon 2026. Ushirikiano huu umewezesha kuokoa maisha ya Watanzania wengi," alisema Bw. Sabi.
Alitoa shukrani maalumu kwa wadhamini wakuu wa mbio hizo akiwemo Sanlam Allianz, GSM Group, Vodacom Tanzania, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) pamoja na wadau wengine waliochangia mafanikio ya tukio hilo.
Katika mbio za kilomita 42 (Full Marathon) kwa upande wa wanaume, mwanariadha kutoka Kenya Edwin Koech aliibuka mshindi wa kwanza kwa kutumia muda wa saa 2:05:12, akifuatiwa na Vitalis Kibiwott aliyemaliza kwa saa 2:12:18.
Kwa upande wa wanawake, Agnes Ngolo wa Kenya alitwaa ushindi kwa kutumia muda wa saa 2:32:36, huku Jacinta Chepkoech, pia kutoka Kenya, akimaliza wa pili kwa muda wa saa 2:33:26.
Washindi wa nafasi ya kwanza hadi ya kumi walizawadiwa fedha taslimu, ambapo washindi wa kwanza wa mbio za kilomita 42 kwa wanaume na wanawake kila mmoja alijishindia Tsh milioni 11.5.
Katika mbio za kilomita 21 (Half Marathon) kwa wanaume, Bernard Geay wa Tanzania aliibuka mshindi wa kwanza kwa muda wa saa 1:02:46, akifuatiwa na Simon Kelenzoke wa Kenya (1:02:57), huku nafasi ya tatu ikichukuliwa na Michael Geay wa Tanzania kwa muda wa 1:02:59.
Kwa upande wa wanawake, Magdalena Shauri wa Tanzania aliibuka mshindi wa kwanza kwa muda wa 1:08:59, akifuatiwa na Doreen Chetzop wa Kenya aliyemaliza kwa muda wa 1:10:36.
Washindi wa kwanza wa mbio za kilomita 21 kwa wanaume na wanawake walijishindia Tsh milioni 5.5, huku washindi wa pili wakiondoka na Tsh milioni 2.5.
NBC Dodoma Marathon imeendelea kuthibitisha kuwa si tu tamasha kubwa la michezo nchini, bali pia ni jukwaa la kuhamasisha afya, kuunganisha jamii, kukuza uchumi wa Jiji la Dodoma na kuchangia moja kwa moja kuboresha huduma muhimu za afya kwa Watanzania.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, (katikati) akimkabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya Tsh milioni 200 kwa muwakilishi wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) (wanne kushoto) iliyotolewa na Benki ya NBC kwa ajili ya kugharamia upasuaji wa watoto wenye matatizo ya moyo kupitia mbio za NBC Dodoma Marathon zilizofanyika leo kwenye Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma. Wanaoshuhudia ni pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Bi. Rosemary Senyamule (wa tatu kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC Bw Theobald Sabi (wa nne kulia), Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya benki ya NBC , Dkt. Elirehema Doriye (wa pili kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa SanlamAllianz, wadhamini wakuu wa mbio hizo, Bw Julius Magabe (kushoto) na viongozi wengine kutoka serikalini na wadau wa mbio hizo.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, (katikati) akimkabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya Tsh milioni 200 kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Benjamin Mkapa, Profesa Abel Makubi (wa tatu kushoto) iliyotolewa na Benki ya NBC kwa ajili ya kusaidia huduma za upandikizaji wa uloto kwa watoto wenye ugonjwa wa selimundu (sicke cell)kupitia mbio za NBC Dodoma Marathon zilizofanyika leo kwenye Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma. Wanaoshuhudia ni pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Bi. Rosemary Senyamule (wa pili kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC Bw Theobald Sabi (wa pili kulia), Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya benki hiyo, Dkt. Elirehema Doriye (kushoto) na viongozi wengine kutoka serikalini na wadau wa mbio hizo.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, (katikati) akimkabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya Tsh milioni 200 kwa muwakilishi wa Taasisi ya Benjamin Mkapa Foundation (wanne kushoto) iliyotolewa na Benki ya NBC kwa ajili ya kwa ajili ya kupanua programu ya ufadhili wa wakunga ili kuboresha huduma za afya ya uzazi kupitia mbio za NBC Dodoma Marathon zilizofanyika leo kwenye Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma. Wanaoshuhudia ni pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Bi. Rosemary Senyamule (wa tatu kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC Bw Theobald Sabi (wa nne kulia), Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya benki ya NBC , Dkt. Elirehema Doriye (wa pili kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa SanlamAllianz, wadhamini wakuu wa mbio hizo, Bw Julius Magabe (kushoto) na viongozi wengine kutoka serikalini na wadau wa mbio hizo.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, (wa tatu kushoto) akikabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya sh mil 5.5 kwa mwanariadha kutoka Tanzania, Magdalena Shauri alieibuka mshindi wa kwanza (kwa upande wa wanawake) wa mbio za km 21 za NBC Dodoma Marathon, zilizofanyika leo kwenye Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma. Wanaoshuhudia ni pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC Bw Theobald Sabi (wa pili kulia) na viongozi wengine kutoka serikalini na wadau wa mbio hizo.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, (kushoto) akikabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya sh mil 11.5 kwa mwanariadha kutoka Kenya, Edwin Koech alieibuka mshindi wa kwanza (kwa upande wa wanaume) wa mbio za km 42 za NBC Dodoma Marathon, zilizofanyika leo kwenye Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma. Wanaoshuhudia ni pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC Bw Theobald Sabi (kulia)














.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
















.jpeg)


.jpeg)


.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)

.jpeg)
