Wananchi wa Mkoa wa Geita wametakiwa kuendelea kudumisha na kuimarisha ushirikiano uliopo kati ya Jeshi la Polisi Jamii na wananchi, ili kupunguza uhalifu katika maeneo mbalimbali mkoani humo.

Wito huo umetolewa leo Agosti 22, 2026 wakati wa maadhimisho ya miaka 20 tangu kuanzishwa kwa mfumo wa Polisi Jamii nchini, yaliyofanyika katika Viwanja vya CCM Kalangalala mjini Geita.=

Akizungumza katika maadhimisho hayo, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhe. Martin Shigela, amesema ushirikiano baina ya wananchi na polisi umekuwa na mchango mkubwa katika kurahisisha mapambano dhidi ya uhalifu mkoani Geita.

"Ushirikiano huu ndio unaotufanya tuweze kupambana na uhalifu kwa urahisi. Tunaposhirikiana, taarifa zinafika kwa wakati na hivyo tunazuia uhalifu kabla haujafanyika," amesema Shigela.

Katika hatua nyingine, Mkuu wa Mkoa amezindua rasmi "Polisi Jamii Run Club mpya ya Mkoa wa Geita. 

Klabu hiyo itakuwa na jukumu la kuhamasisha wananchi kushiriki mazoezi ya kukimbia mbio nyepesi, huku ikiwa na lengo la kuimarisha zaidi uhusiano na ushirikiano kati ya askari na jamii.

Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita,  Safia Jongo, amekiri kuwepo kwa ushirikiano mkubwa kati ya wananchi na jeshi la polisi tangu kuanzishwa kwa falsafa ya Polisi Jamii.

Tumekuwa na ushirikiano mkubwa na jeshi la polisi. Leo hii polisi haogopewi tena mtaani kama zamani ambapo alitumika kutishia watoto. Sasa askari na wananchi ni marafiki katika kulinda usalama," amesema Jongo.

Naye Mratibu wa Polisi Jamii Mkoa wa Geita, Amina Kaando, amesema michezo hiyo inalenga kuunganisha jamii na askari ili wananchi waweze kutambua kuwa askari na jamii ni kitu kimoja katika kuzuia na kupambana na uhalifu.

Maadhimisho ya miaka 20 ya Polisi Jamii Mkoa wa Geita yamedhaminiwa na Mgodi wa Dhahabu GGML. 

Katika maadhimisho hayo, GGML wamefanikiwa kuwakaribisha washiriki wa Jogging kutoka mikoa mingine ikiwemo Kigoma, Shinyanga na Mwanza.










Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewataka viongozi katika ngazi mbalimbali za Serikali kuanza mara moja maandalizi ya kukabiliana na mvua kubwa zinazotarajiwa kunyesha nchini katika kipindi kijacho.

Rais Samia amesema utabiri wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) unaashiria uwezekano wa kuwepo kwa mvua kubwa, hivyo amewataka wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya pamoja na viongozi wa taasisi kuhakikisha maeneo yao yanaweka mikakati madhubuti ya kupunguza athari zinazoweza kujitokeza.

Agizo hilo limetolewa leo, Agosti 22, 2026, wakati Rais Samia akizindua rasmi Mradi wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere (JNHPP) uliopo Rufiji, mkoani Pwani.

Amesisitiza umuhimu wa maandalizi ya mapema, akieleza kuwa viongozi wanapaswa kuhakikisha mifumo ya kukabiliana na majanga iko tayari, huku miundombinu inayoweza kuathiriwa na mvua ikiwekewa ulinzi na hatua stahiki za kuzuia madhara zikichukuliwa kabla ya mvua kuanza.

Kwa mujibu wa Rais Samia, maandalizi hayo yanapaswa kuhusisha ushirikiano wa karibu kati ya Serikali na wananchi ili kuongeza uwezo wa kukabiliana na majanga, kulinda maisha ya watu, mali pamoja na miundombinu muhimu.

Aidha, amewataka wananchi kutopuuza tahadhari zinazotolewa na mamlaka husika, bali kuwa tayari kuchukua hatua za kujilinda na mali zao pale mvua hizo zitakapoanza.

Rais Samia amesisitiza kuwa kukabiliana na athari za mvua kubwa ni jukumu la pamoja, hivyo kila mmoja anatakiwa kutekeleza wajibu wake kwa wakati ili kupunguza uwezekano wa kutokea kwa maafa makubwa.



Na Janeth Raphael - MichuziTv

PWANI: Tanzania imeingia katika hatua mpya ya sekta ya nishati baada ya Kituo cha Kuzalisha Umeme cha Julius Nyerere (JNHPP) kuzinduliwa rasmi, huku mradi huo ukitarajiwa kuwa kichocheo muhimu cha shughuli za kiuchumi na kijamii nchini.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mradi huo leo, Jumamosi, Agosti 22, 2026, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema kukamilika kwa JNHPP ni matokeo ya msimamo wa Serikali wa kuwekeza katika miradi mikubwa yenye uwezo wa kubadilisha mazingira ya uzalishaji na upatikanaji wa umeme nchini.

Rais Samia amesema mradi huo una umuhimu wa kipekee kwa Tanzania kutokana na uwezo wake wa kuongeza uzalishaji wa umeme, akisisitiza kuwa Serikali haikuwa na sababu ya kuacha kuutekeleza kwa kuzingatia mchango wake katika maendeleo ya Taifa.

Rais Samia, amesema hatua ya sasa imefikiwa baada ya safari ndefu ya utekelezaji wa mradi huo, akirejea Desemba 22, 2022 aliposhuhudia hatua ya kufungwa kwa njia ya kuchepusha maji ya Mto Rufiji na kuanza kwa ujazaji wa bwawa.

Amesema awali ilitarajiwa bwawa hilo kujazwa ndani ya kipindi cha takribani miaka mitatu, lakini kutokana na kasi ya ujazaji maji, lilifikia kiwango kilichowezesha majaribio ya uzalishaji wa umeme ndani ya takribani mwaka mmoja na nusu.

Katika ziara yake wakati wa uzinduzi, Rais Samia alikagua miundombinu mbalimbali ya mradi huo, ikiwemo mitambo ya kuzalisha umeme, tuta kuu pamoja na kituo cha kupokea na kusafirisha umeme kwenda kwenye Gridi ya Taifa.

Amesema kuona miundombinu hiyo ikifanya kazi ni hatua kubwa na ya kujivunia kwa Tanzania, hasa kutokana na nafasi ya mradi huo katika kuimarisha uwezo wa nchi kukidhi mahitaji ya umeme yanayoongezeka.

JNHPP ina uwezo wa kuzalisha Megawati 2,115, kiwango kinachoongeza kwa kiasi kikubwa uwezo wa uzalishaji wa umeme nchini.

Ongezeko hilo linatarajiwa kutoa msukumo kwa sekta mbalimbali, ikiwemo viwanda, biashara, uwekezaji na huduma za kijamii, huku upatikanaji wa umeme wa uhakika ukiendelea kuwa msingi muhimu wa ukuaji wa uchumi.

Kwa kukamilika na kuzinduliwa kwa JNHPP, Tanzania sasa inaongeza uwezo wake wa kuzalisha umeme na kuweka mazingira bora zaidi ya kukabiliana na mahitaji ya nishati yanayoendelea kukua.


Na Belinda Joseph – Tanga

Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) imetajwa kuwa moja ya taasisi muhimu katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, kutokana na mchango wake katika kuwaandaa Watanzania wenye ujuzi unaohitajika katika uzalishaji na shughuli mbalimbali za kiuchumi.

Akizungumza na Michuzi TV Agosti 21, 2026, Meneja Mahusiano na Masoko wa VETA, Sitta Peter, amesema VETA itatumia nguzo tatu kwenye utekelezaji wa Dira ya Taifa ambazo ni uchumi imara, jumuishi na shindani, uwezo wa watu na maendeleo ya jamii, pamoja na uhifadhi wa mazingira na ustahimilivu wa mabadiliko ya tabianchi, yanahitaji nguvu kazi yenye ujuzi na umahiri.

Amesema katika kujenga uchumi imara na shindani, Tanzania inahitaji kuongeza tija katika uzalishaji, kuwekeza katika viwanda na kutekeleza miradi mbalimbali ya kiuchumi, ambayo yote yanahitaji wataalamu wenye uwezo wa kufanya kazi kwa ufanisi.

“Tunaposema tufanye uchumi wetu uwe imara na shindani, maana yake tunahitaji kuongeza tija kwenye uzalishaji, tunahitaji uwekezaji kwenye viwanda na tunahitaji utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kiuchumi, haya yote yanahitaji watu wenye ujuzi na umahiri."

Amesema vijana wanaopata mafunzo kupitia VETA wanaweza kunufaika na fursa zinazotokana na ukuaji wa sekta za uzalishaji, viwanda na miradi ya maendeleo kupitia ajira na kujiajiri, huku ujuzi ukiwawezesha pia kuongeza ufanisi katika shughuli kama kilimo na hivyo kuongeza uzalishaji na tija.

Amesema katika kutekeleza nguzo ya uhifadhi wa mazingira na ustahimilivu wa mabadiliko ya tabianchi, VETA tayari imepanda miti 130,800 katika vyuo vyake kote nchini, huku ikiendelea kutekeleza matumizi ya nishati safi ambapo vyuo 26 tayari vinatumia nishati hiyo, ikiwemo gesi na mkaa mbadala.

Ameongeza kuwa Chuo cha VETA Moshi kwasasa kinazalisha mkaa mbadala unaoweza kutumika kama nishati safi, huku kupitia Mradi wa Elimu na Stadi kwa Ajira zenye tija (ESPJ II) VETA ikipanga kuimarisha programu za usimamizi wa taka, matumizi sahihi ya rasilimali, utunzaji wa mazingira pamoja na afya na usalama mahali pa kazi.

Amesisitiza kuwa uwekezaji katika elimu na mafunzo ya ufundi stadi ni muhimu katika kujenga nguvu kazi yenye uwezo wa kuchochea tija, ajira na ukuaji wa uchumi, huku hatua za VETA katika mazingira na matumizi ya nishati safi zikiendelea kuunga mkono utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.



WAFANYAKAZI wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Kanda ya Mashariki wamefanya mazoezi ya kukimbia umbali wa takribani kilomita saba katika eneo la Coco Beach jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya kujiweka katika hali nzuri ya kiafya na utayari wa kutekeleza majukumu yao.

Akizungumza baada ya zoezi hilo leo Agosti 22, 2026 Jijini Dar es Salaam, Mhifadhi Mwandamizi wa TFS, Sunday Nachule, kwa niaba ya Kamanda wa Kanda ya Mashariki, amesema mazoezi hayo ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha askari wanakuwa timamu muda wote kwa ajili ya kutekeleza majukumu yao.

Amesema TFS itaendelea kuhamasisha watumishi wake kushiriki katika mazoezi ya mwili mara kwa mara ili kujenga afya na utayari wa kiutendaji.

Katika zoezi hilo, wanafamilia wa TFS wamepata pia fursa ya kufanya mazoezi pamoja na Mbunge wa Jimbo la Buchosa, Eric Shigongo, ambaye amewapongeza kwa juhudi hizo na kuwataka kuendelea na mazoezi.

Shigongo amesema misitu ni muhimu kwa uhai wa binadamu kutokana na mchango wake katika upatikanaji wa hewa safi na maji, hivyo wananchi wanapaswa kushirikiana na Serikali katika kuilinda.

Ametaja maeneo ya Buhindi na Lubondo yaliyopo katika Jimbo la Buchosa kuwa miongoni mwa maeneo yenye misitu inayosimamiwa na TFS, akisisitiza umuhimu wa wananchi kutunza rasilimali hiyo.

“Bila misitu hakuna uhai. Kwa hiyo nawaomba Watanzania waendelee kutunza misitu kwa sababu ni chanzo cha hewa na maji,” amesema Shigongo.

Aidha, ameipongeza TFS kwa kazi inayofanya katika kulinda na kuhifadhi misitu nchini, akieleza kuwa wananchi wanapaswa kuwa wadau wa uhifadhi kwa kuhakikisha rasilimali hiyo inalindwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.











Manyara Tanzanite Marathon 2026, mbio za hisani zenye lengo la kuchangisha fedha kwa ajili ya ujenzi na uwezeshaji wa wodi maalum ya kuwahudumia watoto njiti, zimefanyika leo katika Mji wa Babati, zikiwa na kaulimbiu “Hatua Moja, Okoa Maisha ya Mtoto Njiti.”

Mbio hizo za hisani zimeongozwa na Mgeni Rasmi kwa niaba ya Waziri Mkuu, Mhe. Mwigulu Nchemba, Naibu Spika wa Bunge, Mhe. Daniel Sillo, ambaye amempongeza Mkuu wa Mkoa wa Manyara kwa ubunifu wa kuanzisha Manyara Tanzanite Marathon, akieleza kuwa mbio hizo ni sehemu ya jitihada za kuchangia moja kwa moja katika kuokoa maisha ya watoto njiti.

Manyara Tanzanite Marathon 2026 inalenga kukusanya jumla ya shilingi bilioni 1.5, fedha zitakazotumika katika ujenzi na uwezeshaji wa wodi maalum kwa ajili ya kutoa huduma kwa watoto wanaozaliwa kabla ya wakati.

Mbio hizo zimewakutanisha wananchi na wanariadha kutoka maeneo mbalimbali, katika kuunga mkono juhudi za kuboresha huduma za afya na kuokoa maisha ya watoto njiti.

Mbio za Hisani za Manyara Tanzanite Marathon zimefanyika leo mkoani Manyara, zikihudhuriwa na watu mbalimbali kutoka maeneo tofauti ya nchi pamoja na viongozi mbalimbali, huku lengo kuu likiwa ni kuchangisha fedha kwa ajili ya kuokoa maisha ya watoto wachanga na watoto njiti.
Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Daniel Sillo, aliyemwakilisha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye alitarajiwa kuwa mgeni rasmi katika mbio hizo, amepongeza uongozi wa Mkoa wa Manyara kwa ubunifu wa kuanzisha mbio hizo zinazolenga kuchangisha fedha kwa ajili ya kuimarisha huduma za afya na kuokoa maisha ya watoto wachanga na watoto njiti.

Sillo amesema hatua hiyo ni mfano wa ubunifu unaopaswa kuigwa na maeneo mengine nchini, akisisitiza umuhimu wa kushirikisha jamii na wadau katika kusaidia kuboresha huduma za afya.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa TAMISEMI, Jafari Rajabu, amesema mbio hizo zimeleta tija kubwa katika juhudi za kuokoa maisha ya watoto, akiwataka wananchi na wadau kuendelea kuunga mkono jitihada zinazolenga kuboresha afya ya watoto.

Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, amewashukuru wadau wote walioshiriki na kuunga mkono maandalizi ya mbio hizo, akisema ushiriki wao umewezesha kufanikisha azma ya kuchangisha fedha kwa ajili ya watoto wanaohitaji huduma maalumu za afya.

Baadhi ya washiriki wa mbio hizo wamesema, pamoja na kushiriki kwa ajili ya mazoezi na kuimarisha afya zao, wameona umuhimu wa kuwa sehemu ya harakati za kuchangia maisha ya watoto wachanga na watoto njiti.

Wamesema ushiriki wao katika Manyara Tanzanite Marathon umewapa fursa ya kufanya mazoezi huku wakitoa mchango wa moja kwa moja katika kusaidia kuokoa maisha ya watoto, hivyo kuwataka wananchi wengine kuendelea kushiriki katika matukio yenye malengo ya kijamii na kiafya.




































 


Top News