Na Mwandishi Wetu
WAZIRI Wa Elimu Sayansi Na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda anatarajiwa kuzindua wiki ya elimu,ujuzi na ubunifu inayoendelea katika viwanja vya shule ya sekondari jijini Tanga kesho Agosti 18,2026.

Mkuu wa mkoa huo, Batilda Buriani amesema hayo alipotembelea maonesho hayo na kuongeza kuwa washiriki zaidi ya 300 wapo katika wiki hiyo ambao tayari wamepanga bunifu mbalimbali katika mabanda pamoja na kutoa elimu.

Amewahakikishia wananchi usalama na ulinzi wakati wote wa maonesho na kwamba wanakaribishwa kufika kwa wingi katika viwanja hivyo ili kujifunza kaa kuwa taasisi zote za elimu zikonkatika viwanja hivyo pamoja na taasisi za utafiti.

“Kwa muda wote wa wiki moja kuanzia Agosti 15,2026 hadi Agosti 24,2026 maadhimisho yataanza saa mbili asubuhi na kufugungwa jioni saa 12”, amesema Burian na kuongeza kuwa Waziri Mkuu,Dk Mwigulu Nchemba anatarajiwa kufunga maonesho hayo yenye kauli mbiu elimu,jjuzi,ubunifu njiabya kufikia dira ya Taifa 2050.

Batilda ameongeza kuwa washirikinkatika maonesho hayo ni pamoja na vyuo vikuu,tasisi za tafiti ,vyuo vya elimu na ufundi stad na taasisi binafsi ambazo zinahusiana na sayansi na teknolojia.

Amewataka wananchi kutembelea maonesho hayo kwa kuwa ni nafasi ya pekee kujifunza mambo mbakimbali hara kwa wale wanaotafuta vyuo na usajili.

Na Mwandishi Wetu, Tanga
MAWAZO ya ubunifu na teknolojia yanayobuniwa na wanafunzi na wahitimu wa Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) yameelezwa kuwa ni fursa muhimu kwa vijana kujiajiri, huku yakitoa suluhisho la changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi.

Miongoni mwa wabunifu hao ni Calven Mwakampya, mhitimu wa TIA ambaye amebuni kifaa cha teknolojia kinachoitwa Smart Glove, kinachowezesha mawasiliano kati ya mtu mwenye uziwi na asiye na uziwi.

Mwakampya amebuni mfumo unaotumia vitufe vya alama za mawasiliano, ambapo ujumbe unaowasilishwa na mtu mwenye uziwi unaweza kubadilishwa kuwa sauti na kusikika kwa mtu asiye na uziwi, hivyo kusaidia kuondoa changamoto ya mawasiliano kati ya makundi hayo.

Akizungumza katika Maonesho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanayoendelea katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara jijini Tanga, Mwakampya alisema ubunifu huo wa kiteknolojia umemsaidia kutengeneza suluhisho la changamoto ya mawasiliano inayowakabili watu wenye uziwi.

Alisema amekuwa miongoni mwa wahitimu walionufaika na mpango wa TIA wa kukuza na kuendeleza vipaji na taaluma, jambo lililomsaidia kuboresha wazo lake na hatimaye kuanzisha kampuni.

"Nimekuwa miongoni mwa wanafunzi wanaonufaika na mpango wa TIA wa kukuza na kuendeleza vipaji na taaluma, jambo linalonisaidia kuendeleza wazo ambalo sasa tumeanzisha kampuni," alisema Mwakampya.

Alisema TIA imekuwa ikimpa mwongozo na usimamizi katika kuboresha ubunifu huo, ambao umeanza kuwa suluhisho la changamoto zinazowakabili watu wenye uziwi katika mawasiliano.

Kwa mujibu wa Mwakampya, mfumo huo utamwezesha mtu mwenye uziwi kuwasiliana na mtu asiye na uziwi kwa urahisi, huku ujumbe wa alama ukibadilishwa kuwa sauti ili kumwezesha mtu asiye na uziwi kuelewa mahitaji ya anayewasiliana naye.

Alisema mfumo huo pia utasaidia kuongeza ufanisi wa mawasiliano kati ya jamii ya watu wenye uziwi na wasio na uziwi katika maeneo mbalimbali ya huduma za kijamii.

Mwakampya alisema matumizi ya teknolojia katika sekta ya mawasiliano ni muhimu katika kuhakikisha watu wenye uziwi wanapata na kutoa huduma kwa ufanisi kama ilivyo kwa watu wasio na uziwi.

Aidha, alisema mpango wa TIA wa kuendeleza mawazo na ubunifu wa wanafunzi una nafasi kubwa katika kuongeza fursa za ajira, hususani kwa vijana wanaohitimu katika vyuo mbalimbali.

"Ubunifu unaotokana na wanafunzi unaweza kuwa chanzo cha kujiajiri na pia kutoa suluhisho la changamoto mbalimbali zinazolikabili Taifa," alisema.

Alitoa wito kwa vijana kutumia maarifa wanayopata vyuoni kubuni teknolojia na bidhaa zitakazokuwa na manufaa kwa jamii, badala ya kutegemea ajira baada ya kumaliza masomo.

"Ninatoa wito kwa vijana kutumia maarifa wanayopata vyuoni kubuni teknolojia zitakazokuwa na manufaa kwa jamii," alisema Mwakampya.

Alisema miongoni mwa wadau wanaoweza kunufaika na teknolojia hiyo ni TIA kwa ajili ya kusaidia katika ufundishaji wa watu wenye uziwi, Chama cha Viziwi Tanzania (CHAVITA), hospitali na maeneo mengine ya kutolea huduma.

Na Mwandishi Wetu, Tanga
MAMLAKA ya Elimu Tanzania (TEA) imesema mkondo wa Amali katika shule za sekondari umeendelea kupata mwitikio mkubwa kutoka kwa wanafunzi kutokana na upatikanaji wa vifaa vinavyowawezesha kujifunza kwa vitendo.

Akizungumza katika Maonesho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanayoendelea katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara jijini Tanga, Afisa Miradi wa TEA, Kabula Julu, alisema shule zilizofadhiliwa vifaa kwa ajili ya mkondo wa Amali zimeanza kushuhudia ongezeko la hamasa miongoni mwa wanafunzi.

Alisema miongoni mwa shule zilizonufaika na ufadhili huo ni Shule ya Sekondari ya Wasichana Korogwe, ambayo imepatiwa vifaa vyenye thamani ya zaidi ya Sh milioni 400 kwa ajili ya kufundishia fani tano.

Alizitaja fani hizo kuwa ni Upishi, Kilimo cha Mboga na Matunda, Ushonaji, Kilimo cha Mazao ya Chakula pamoja na Afya ya Wanyama.

Julu alisema shule nyingine zilizonufaika na ufadhili wa TEA ni pamoja na Uwemba, Iringa, Kigoma, Dar es Salaam, Arusha, Chief Salwart ,Morongo pamoja na Korogwe.

Alisema miongoni mwa shughuli zinazotekelezwa na TEA ni kufadhili shule zenye mkondo wa Amali, ambao umekuwa ukipata mwitikio mkubwa kutokana na kuwawezesha wanafunzi kujifunza kwa vitendo zaidi badala ya kutegemea nadharia pekee.

"Tumefadhili shule zenye mkondo wa Amali na mwitikio umekuwa mkubwa, kwa sababu wanafunzi wana uhitaji wa kujifunza kwa vitendo zaidi kuliko nadharia," alisema Julu.

Aliongeza kuwa ushiriki wa TEA katika maonesho hayo unatoa fursa kwa wananchi kufahamu namna Mamlaka hiyo inavyoshiriki kuboresha mazingira ya elimu na kuwawezesha wanafunzi kupata ujuzi unaoweza kuwasaidia katika maisha na kujiajiri.

Kwa upande wake, Mwalimu wa Shule ya Sekondari ya Wasichana Korogwe, Catherine Machugu, alisema ufadhili wa TEA umeongeza chachu kwa wanafunzi kupenda na kusoma mkondo wa Amali.

Alisema kabla ya shule hiyo kupata vifaa, wanafunzi walikuwa wakijifunza zaidi kwa nadharia, lakini baada ya kupata vifaa wameanza kujifunza kwa vitendo na matokeo yameanza kuonekana.

"Wakati tulipokuwa hatuna vifaa, wanafunzi walijifunza zaidi kwa nadharia, lakini kwa sasa wanajifunza kwa vitendo na matokeo yanaonekana," alisema Machugu.






MRADI wa Mafunzo ya Kitaaluma ya Ufundi Stadi katika Sekta ya Migodi (IMTT) umeendelea kuwa daraja muhimu kwa vijana kupata ujuzi unaohitajika katika sekta ya migodi, huku mfumo wake wa Uanagenzi ukiwawezesha wanafunzi kujifunza darasani na kufanya kazi za vitendo katika migodi, hatua inayochangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ya kujenga uchumi jumuishi unaoshirikisha wananchi katika shughuli za uzalishaji.

Akizungumza na Michuzi TV katika Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea jijini Tanga kuanzia Agosti 15 hadi 24, Mkufunzi na Mratibu wa Uanagenzi wa IMTT kutoka VETA Moshi, mkoani Kilimanjaro, Mwl. John Nathan, amesema mpango huo ulianzishwa kwa ushirikiano kati ya VETA na Chemba ya Migodi Tanzania yaani (TCM).

Amebainisha kuwa tofauti na mafunzo ya kawaida ya darasani, mradi wa IMTT unafanyika katika mazingira mawili muhimu ni chuoni na katika eneo la kazi kwa maana ya viwandani, na Mfumo huo unamwezesha mwanafunzi kupata maarifa ya kinadharia na ujuzi wa vitendo kwa wakati mmoja, hivyo anapohitimu huwa tayari ana uzoefu wa mazingira halisi ya kazi.

“Anapokwenda kwenye kazi, anakuwa si mgeni tena, hahitaji uzoefu mwingine wa ziada ili kukidhi mahitaji ya ajira kwa sababu tayari ana uzoefu uliojengwa kutokana na muundo wa mafunzo".

Amesema kwa sasa, IMTT inatolewa katika chuo cha VETA Moshi peke yake, hii ni baada ya tafiti za awali zilifanyika na kubaini kuwa chuo hicho kilikuwa na mazingira, vifaa na miundombinu iliyohitajika kuendesha mafunzo hayo. Hata hivyo baadhi ya kampuni za migodi zimekuwa zikisaidia vijana kutoka maeneo yanayozunguka migodi kusafiri hadi Moshi kwa ajili ya mafunzo kabla ya kurejea katika maeneo yao ya kazi.

Ameeleza kuwa kwa mtu yeyote anayehitaji kujiunga na IMTT anatakiwa kuwa na ufaulu wa Kidato cha Nne na kuwa mzawa wa Tanzania na taarifa zaidi kuhusu taratibu za kujiunga wanaweza kufika VETA Moshi au kupata taarifa kupitia tovuti ya VETA.

Kwa upande wa mafanikio, amesema zaidi ya vijana 1,668 wamepatiwa mafunzo kupitia IMTT tangu kuanzishwa kwake mwaka 2009, ambapo asilimia 79.1 wameajiriwa katika migodi mbalimbali nchini, huku asilimia 1.1 wamepata ajira katika migodi nje ya nchi hali inayoonesha kuwa mafunzo ya ufundi stadi yanaweza kuwa njia muhimu ya kuwawezesha vijana kupata ajira.

Akieleza mchango wa programu hiyo katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, amesema IMTT inawawezesha vijana kushiriki moja kwa moja katika sekta ya migodi kwa kuwapatia ujuzi unaowawezesha kuwa sehemu ya nguvu kazi yenye tija, ambapo ajira wanazopata vijana hao haziwanufaishi wao pekee, bali pia familia zao na jamii zinazowazunguka.

Aidha, amegusia mabadiliko ya teknolojia katika sekta ya migodi yameifanya VETA kuendelea kuboresha mitaala ili kukidhi mahitaji mapya, hususan katika uchimbaji wa chini ya ardhi, amesema wanatarajia kuja na Programu sita mpya ambazo ni Scoop Operation, Tele-remote Bogger Operation, Cubex Operation, Jumbo Operation, Lifting and Rigging pamoja na Mobile Charging Unit Operation ili kuongeza ujuzi wa vijana wataokwenda kuisaidia sekta ya migodi kikamilifu kulingana na kasi ya ukuaji wa teknolojia.

Akitoa ujumbe kwa vijana wanaotembelea Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayofanyika katika viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara jijini Tanga, aliwataka kutumia fursa hiyo kupata taarifa kuhusu mafunzo ya ufundi stadi na kuchukua hatua badala ya kubaki na ndoto bila kuzifanyia kazi.

“Usiwe na wazo kichwani ukabaki na wazo, fanyia kazi, anza sasa,” akieleza kuwa vijana waliopitia IMTT wameweza kufikia fursa mbalimbali za ajira ndani na nje ya nchi, jambo linaloonesha kuwa ujuzi wa ufundi unaweza kuwa msingi wa mafanikio ya kiuchumi kwa vijana.




Na Mwandishi Wetu
JUMUIYA ya Wanawake katika Nyuklia Tanzania (WiNTz) imetembelea Hospitali ya KCMC na kufanya mazungumzo na wanawake wanaofanya kazi katika Kitengo cha Tiba ya Mionzi, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Jumuiya hiyo kuwawezesha wanawake katika sekta ya sayansi na teknolojia ya nyuklia kupata fursa za masomo na mafunzo ya muda mfupi na muda mrefu ndani na nje ya nchi.

Ziara hiyo imelenga pia kuwajengea uwezo wanawake wanaofanya kazi katika eneo la tiba ya mionzi kwa kuwafungulia fursa mbalimbali za kitaaluma zitakazowawezesha kuongeza maarifa na ujuzi katika taaluma zao na hivyo kuboresha zaidi huduma wanazozitoa kwa wananchi.

WiNTz, inayoongozwa na Rais wake ambaye pia ni Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC), Prof. Najat Kassim Mohammed, imeendelea kutekeleza programu mbalimbali zinazolenga kuongeza ushiriki wa wanawake na wasichana katika sayansi na teknolojia ya nyuklia nchini.

Miongoni mwa maeneo ambayo Jumuiya hiyo imekuwa ikiyapa kipaumbele ni kuhamasisha wasichana kusoma masomo ya sayansi, kutoa elimu kwa jamii kuhusu umuhimu wa uchunguzi wa saratani mapema, pamoja na kuwaunganisha wanawake wanaosoma na kufanya kazi katika taaluma za sayansi na fursa za masomo, tafiti na mafunzo ya kitaaluma ndani na nje ya Tanzania.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mkaguzi wa Vyanzo vya Mionzi kutoka Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC), Bi. Lucy Lway, amesema pamoja na kukutana na wanawake wanaofanya kazi katika Kitengo cha Tiba ya Mionzi, WiNTz imetumia ziara hiyo kuwafariji watoto wanaopata matibabu ya saratani katika Hospitali ya KCMC.

Amesema Jumuiya hiyo inaamini kuwa pamoja na kuendeleza taaluma na kuwajengea uwezo wanawake katika sekta ya nyuklia, ni muhimu pia kutumia nafasi hiyo kuigusa jamii, hususan wagonjwa wanaopitia vipindi virefu vya matibabu.

Kwa upande wake, Mtaalamu wa Maabara kutoka TAEC, Bi. Hellen Kiyengo, amesema kujenga uelewa sahihi kuhusu teknolojia ya nyuklia ni muhimu katika kuisaidia jamii kufahamu matumizi na manufaa yake katika maisha ya kila siku, ikiwemo nafasi yake katika sekta ya afya.

Amesema elimu sahihi inasaidia pia kuondoa dhana potofu kuhusu teknolojia ya nyuklia na kuwajengea wananchi uelewa wa umuhimu wa kuzingatia usalama wakati wa matumizi ya mionzi.

Naye Msimamizi wa Wodi ya Watoto wanaopata matibabu ya saratani katika Hospitali ya KCMC, Bwn. Robert Kessy, ameipongeza WiNTz kwa kutenga muda wa kuwatembelea watoto wanaopata matibabu ya saratani, akisema baadhi yao hulazimika kukaa hospitalini kwa muda mrefu kutokana na aina na hatua mbalimbali za matibabu wanayopatiwa.

Amesema kutembelewa na kupata faraja kutoka kwa watu na taasisi mbalimbali kunasaidia kuwapa moyo watoto hao pamoja na wazazi na walezi wao katika kipindi cha matibabu.

“Watoto hawa wanakaa hospitalini kwa muda mrefu wakipatiwa matibabu. Kitendo cha Jumuiya ya Wanawake katika Nyuklia Tanzania kutenga muda na kuja kuwaona ni jambo jema kwa sababu kinawapa moyo watoto pamoja na wazazi wao,” amesema Kessy.

Kwa upande wake, Daktari kutoka Kitengo cha Tiba ya Mionzi KCMC, Dkt. Vaileth Mteta, ameishukuru WiNTz kwa kukutana na wanawake wanaofanya kazi katika kitengo hicho, akisema hatua hiyo imewapa nafasi ya kufahamu zaidi kuhusu Jumuiya hiyo pamoja na fursa zinazoweza kupatikana kupitia mtandao wa wanawake wanaofanya kazi katika maeneo ya sayansi na teknolojia ya nyuklia.

Amesema mkutano huo umeongeza pia hamasa ya kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa uchunguzi wa saratani mapema na kuwahi kupata matibabu kabla ugonjwa haujaenea na kufikia hatua ambazo matibabu yake yanaweza kuwa magumu zaidi.

Aidha, amesema wanawake wanaofanya kazi katika Kitengo cha Tiba ya Mionzi wamepata fursa ya kufahamu namna wanavyoweza kujiunga na WiNTz na kutumia mtandao huo kujenga mahusiano ya kitaaluma, kubadilishana uzoefu na kufikia fursa mbalimbali za mafunzo na maendeleo ya taaluma.

Ziara hiyo ni sehemu ya jitihada za WiNTz za kujenga mtandao mpana wa wanawake katika sayansi na teknolojia ya nyuklia nchini, huku ikisisitiza umuhimu wa kuwajengea uwezo wanawake waliopo katika sekta hiyo na kuandaa kizazi kipya cha wasichana wenye ari ya kusomea masomo ya sayansi.

Kupitia shughuli hizo, WiNTz inalenga kuhakikisha wanawake wanasayansi nchini hawapati tu nafasi ya kushiriki katika maendeleo ya teknolojia ya nyuklia, bali pia wanakuwa sehemu muhimu ya kutumia sayansi hiyo katika kutatua changamoto za jamii, hususan katika afya, utafiti na maendeleo ya Taifa.


Na Karama Kenyunko, Michuzi Tv
CHUO Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) kinaandaa mpango wa kuanzisha mafunzo ya wahudumu wa huduma za dharura watakaotoa huduma ya kwanza, ikiwemo usimamizi wa ajali, kuhakikisha njia ya hewa inabaki wazi na kumstabilisha mgonjwa kabla ya kufikishwa hospitalini.

Makamu Mkuu wa MUHAS, Prof. Apollinary Kamuhabwa, amesema hayo leo Agosti 18, 2026, Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa kitengo maalumu cha matibabu ya meno kwa watoto wanaohitaji dawa za usingizi au ganzi, sambamba na kusainiwa kwa hati ya makubaliano (MoU) kati ya MUHAS, Chuo Kikuu cha Ankara na Shirika la Ushirikiano na Uratibu la Türkiye (TİKA).

Amesema mpango huo ni sehemu ya ushirikiano katika huduma za tiba za dharura, ambapo MUHAS imepokea gari la wagonjwa linalotumika kutoa huduma na kuwafundisha wanafunzi.

Amesema chuo hicho kinaandaa mpango wa kuanzisha mafunzo ya wahudumu wa huduma za dharura watakaotoa huduma ya kwanza, ikiwemo usimamizi wa ajali, kuhakikisha njia ya hewa inabaki wazi na kumstabilisha mgonjwa kabla ya kufikishwa hospitalini.

Alisema mpango huo ni muhimu zaidi wakati Tanzania, Kenya na Uganda zikijiandaa kwa pamoja kuandaa Fainali za AFCON 2027.

Mkurugenzi wa TİKA nchini Tanzania, Halim Ömer, amesema mpango wa kuanzisha shule ya wahudumu wa huduma za dharura utajengwa juu ya mafunzo ya kukabiliana na majanga na dharura yaliyotolewa mwaka 2024, ambapo zaidi ya madaktari 50 wa huduma za dharura walipatiwa mafunzo.

Amesema shule hiyo itasaidia kuandaa wataalamu wenye sifa na kuimarisha uwezo wa Tanzania wa kukabiliana na dharura kwa muda mrefu.

Ömer amesema TİKA imetekeleza zaidi ya miradi 350 ya ushirikiano nchini Tanzania katika sekta mbalimbali, ikiwemo elimu, kilimo, mifugo, afya, mafunzo ya ufundi, maji na usafi wa mazingira.

Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo Kikuu cha Ankara, Prof. Dkt. Necdet Ünüvar, amesema ushirikiano katika tiba za dharura ni hatua muhimu katika kuimarisha uhusiano wa kitaaluma na kitaalamu kati ya taasisi hizo, huku akiahidi kupanua ushirikiano katika sayansi za afya.

Prof. Kamuhabwa amesema MoU iliyosainiwa haijaweka kiwango maalumu cha fedha, bali imeweka msingi wa taasisi hizo kuandaa na kutekeleza miradi ya pamoja na kutafuta fedha kutoka TİKA na washirika wengine wa maendeleo


Na Karama Kenyunko, Michuzi Tv
CHUO Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) kimeanzisha kitengo maalumu cha matibabu ya meno kwa watoto wanaohitaji dawa za usingizi au ganzi, ikiwa ni sehemu ya ushirikiano kati ya MUHAS, Chuo Kikuu cha Ankara na Shirika la Ushirikiano na Uratibu la Türkiye (TİKA).

Makamu Mkuu wa MUHAS, Prof. Apollinary Kamuhabwa, amesema hayo leo Agosti 18, 2026, Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa kitengo hicho sambamba na kusainiwa kwa hati ya makubaliano (MoU) kati ya taasisi hizo.

Amesema kitengo hicho kilichoanzishwa katika Shule ya Meno ya MUHAS kimeanza kutoa huduma kwa watoto wenye matatizo ya kinywa na meno ambao hawawezi kufanyiwa matibabu wakiwa macho, huku watoto 27 wakiwa tayari wamepatiwa huduma tangu Mei mwaka huu.

Prof. Kamuhabwa amesema huduma hiyo ni muhimu kwa watoto wanaoogopa sindano, wasioweza kuvumilia matibabu ya meno wakiwa macho au wenye changamoto za kiafya zinazofanya matibabu ya kawaida kuwa magumu.

Amesema huduma hiyo haikuwahi kupatikana nchini, hivyo ushirikiano huo umeleta hatua muhimu katika kuongeza huduma za kibingwa kwa watoto.

“Wataalamu wa MUHAS, wakiwemo madaktari wa meno, wataalamu wa usingizi na ganzi, maabara na wauguzi, wamekwenda Chuo Kikuu cha Ankara kwa mafunzo, huku wataalamu kutoka Türkiye wakifika Tanzania kwa ajili ya kujenga uwezo wa wataalamu wa ndani,” amesema.

Pia TİKA na Chuo Kikuu cha Ankara vimeunga mkono mpango huo kwa kutoa vifaa tiba na utaalamu, huku hatua inayofuata ikiwa ni kuongeza wataalamu, vifaa na kupanua huduma ili watoto wengi zaidi wanufaike.

Mkurugenzi wa TİKA nchini Tanzania, Halim Ömer, amesema TİKA imewezesha kitengo hicho kwa kutoa vifaa vya ganzi, meno, kusaidia njia ya hewa kwa watoto, vifaa vya kupumulia na vifaa vya huduma za dharura

Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo Kikuu cha Ankara, Prof. Dkt. Necdet Ünüvar, amesema kuanzishwa kwa kitengo hicho ni hatua muhimu katika kuimarisha uhusiano wa kitaaluma na kitaalamu kati ya taasisi hizo, huku akiahidi kupanua ushirikiano katika sayansi za afya.

Mkuu wa Shule ya Meno ya MUHAS, Prof. Ferdinand Machibya, amesema ushirikiano huo unaweza kupanuliwa katika utafiti wa pamoja, mafunzo ya uzamili, kubadilishana wanafunzi na wataalamu, matumizi ya akili bandia katika uchanganuzi wa picha za kitabibu, kujenga uwezo wa huduma za tiba na kuandaa maombi ya pamoja ya ruzuku.

Na Janeth Raphael – MichuziTv

MFUKO wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) umeweka mkakati wa kuhakikisha kaya zitakazonufaika na Mpango wa Tatu wa TASAF zinatumia fursa zitakazotolewa kujijengea uwezo wa kiuchumi na hatimaye kuondokana na utegemezi ndani ya kipindi cha miaka mitatu kabla ya kuhitimu kwenye mpango huo.

Mpango huo unatekelezwa kwa kipindi cha miaka minne, kuanzia mwaka 2026 hadi 2030, ukiwa na lengo la kubadilisha maisha ya kaya maskini kwa kuzipatia fursa za kuongeza kipato, kuimarisha uwezo wa kujitegemea na kujenga msingi wa maendeleo endelevu, badala ya kuendelea kutegemea msaada kwa muda usio na ukomo.

Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF, Shadrack Mziray, amesema hayo wakati wa ziara ya Kamati ya Baraza la Wawakilishi inayosimamia Ofisi za Viongozi Wakuu wa Kitaifa Zanzibar, iliyotembelea Makao Makuu ya TASAF jijini Dodoma.

Mziray amesema mkakati huo unalenga kuhakikisha kaya zinazonufaika na mpango zinatumia ipasavyo fursa zinazotolewa katika kipindi cha miaka mitatu, kabla ya kuhitimu na kuendelea na maisha ya kujitegemea kiuchumi.

Amesema baada ya kaya kuhitimu, TASAF itaendelea kuzifuatilia ili kutathmini maendeleo yake na kuhakikisha zinabaki katika hali ya kujitegemea kiuchumi.

“Lengo letu ni kuona kaya zinatumia fursa hii kama daraja la kutoka kwenye utegemezi na kujenga uwezo wa kujitegemea. Tunataka wanufaika waweze kuongeza kipato na kuboresha maisha yao kwa njia endelevu,” amesema Mziray.

Kwa upande wa mmoja wa  wajumbe wa Kamati hiyo ameishauri TASAF kuendelea kuimarisha mifumo ya ufuatiliaji na tathmini ya utekelezaji wa Mpango wa Tatu, ili kuhakikisha malengo yaliyowekwa yanafikiwa na kaya zinazonufaika zinapata matokeo yaliyokusudiwa.

Wajumbe hao wameeleza kuwa ufuatiliaji wa karibu ni muhimu katika kuhakikisha fursa zinazotolewa kwa kaya maskini zinatumika ipasavyo na kuleta mabadiliko ya kiuchumi na kijamii kwa wanufaika.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Machano Othman Said, amepongeza TASAF kwa mchango wake katika juhudi za kupunguza umaskini nchini, akisema programu hiyo imeendelea kuwa chachu ya kuwapatia wananchi wa Tanzania Bara na Zanzibar fursa za kuboresha maisha yao.

Machano amesema juhudi za TASAF zimekuwa muhimu katika kuwawezesha wananchi wenye uhitaji kupata fursa zinazowasaidia kuongeza kipato na kujenga uwezo wa kukabiliana na changamoto za kiuchumi.

Utekelezaji wa Mpango wa Tatu wa TASAF unatarajiwa kugharimu zaidi ya Dola za Marekani milioni 650 na unalenga kunufaisha zaidi ya kaya milioni 1.5 zenye uhitaji Tanzania Bara na Zanzibar.

Kupitia mpango huo, TASAF inalenga kuhakikisha uwekezaji unaofanyika kwa kaya maskini hauishii katika kutoa msaada wa muda mfupi, bali unatumika kama msingi wa kuwawezesha wanufaika kuongeza kipato, kujenga uwezo wa kiuchumi na hatimaye kuondokana na utegemezi.







Katibu wa NEC, Uchumi na Fedha wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Jamal Kassim Ali, amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Uchumi Tanzania (TISEZA), Ndugu Gilead John Teri, kuhusu fursa za kimkakati za uwekezaji na namna ya kuongeza mchango wa sekta binafsi katika kukuza uchumi wa Taifa.

Mazungumzo hayo yaliyofanyika katika Ofisi Ndogo za CCM, Lumumba, Dar es Salaam, yalijikita katika maeneo yenye kuchochea ukuaji wa uchumi na kuongeza mapato, ikiwemo uchukuzi na usafirishaji, madini, ardhi na majengo (real estate), pamoja na uwekezaji katika maeneo yenye fursa za kiuchumi.

Pande hizo pia zilijadili namna CCM inavyoweza kuendelea kuendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na kutekeleza kwa ufanisi vipaumbele vilivyoainishwa katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2025–2030, hususan katika kukuza uwekezaji, uzalishaji, ajira na mapato.

Akizungumza katika kikao hicho, Ndugu Jamal alisisitiza umuhimu wa Chama kuwa na mtazamo wa muda mrefu katika kutambua na kutumia fursa za uwekezaji zilizopo nchini.

Alisema ushirikiano kati ya Chama, taasisi za Serikali, wawekezaji na sekta binafsi ni muhimu katika kuhakikisha fursa zilizopo zinabadilishwa kuwa shughuli halisi za kiuchumi zenye tija na manufaa kwa Taifa.

Mazungumzo hayo ni sehemu ya juhudi za CCM za kuimarisha ushirikiano na wadau wa uchumi na uwekezaji, kwa lengo la kuongeza ufanisi, mapato na mchango wa rasilimali za Chama katika maendeleo ya Taifa.




Naibu Katibu Mkuu CCM Zanzibar, Ndg. Abdi Mahamoud Abdi, amewataka viongozi na watendaji wa chama katika ngazi zote kufanya kazi kwa bidii, mshikamano na ushirikiano wa pamoja ili kuhakikisha Chama Cha Mapinduzi kinaendelea kupata matokeo chanya katika utekelezaji wa majukumu yake.

Ndg. Abdi ameyasema hayo leo, Agosti 17, 2026, katika ukumbi wa Jengo la Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui, Zanzibar, wakati akizungumza katika kikao cha pamoja kilichowakutanisha viongozi na watendaji wa CCM, Jumuiya ya Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), Jumuiya ya Wazazi pamoja na watendaji wa Afisi Kuu ya CCM Zanzibar.

Amesema kila mtendaji wa chama ana jukumu la kuhakikisha anatekeleza majukumu yake kwa bidii, uadilifu na kwa kuzingatia wajibu aliopewa katika kitengo chake, huku akisisitiza umuhimu wa kudumisha ushirikiano na watendaji wenzake.

Ndg. Abdi amesema mafanikio ya chama yanategemea kwa kiasi kikubwa namna viongozi na watendaji wake wanavyoshirikiana katika kutekeleza majukumu yao, hivyo amewataka kuacha kufanya kazi kwa misingi ya mtu mmoja mmoja na badala yake kujenga utamaduni wa kufanya kazi kwa pamoja.

Aidha, Naibu Katibu Mkuu huyo amewatoa hofu watendaji wa chama kuhusu masuala ya maslahi yao, akisisitiza kuwa ataendelea kusimamia kikamilifu maslahi yao ili kuwawezesha kuwa na mazingira bora yatakayowapa motisha ya kufanya kazi kwa bidii na kwa ufanisi zaidi.

Amesisitiza kuwa watendaji wanapaswa kutumia nafasi zao kwa kutekeleza majukumu ya chama kwa ufanisi, huku wakilinda umoja, mshikamano na misingi ya Chama Cha Mapinduzi.









 

Na Mwandishi Wetu

SERIKALI  imeombwa kuzipa nafasi kampuni zenye uwezo wa kuzalisha gesi ya Okseji ambayo inajukulikana kwa jina la hewa tiba kwa  ajili ya matumizi ya hospitalini kwa kuwa kampuni hizo zinauwezo mkubwa na zimebobea katika uzalishaji huo.

Ombi hilo limetolewa leo jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya TOL Gases PLC Daniel Warungu alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari baada ya kumalizika kwa Mkutano Mkuu wa 31 wa mwaka wa Wanahisa huku akisisitiza wao wamekuwa na uwezo mkubwa wa kuzalisha.

Amesema kwa sekta binafsi zinazalisha gesi ya Oksijeni hivyo ni vema Serikali ikawa inanunua badala ya kuzalisha na kupikia mitambo huku akifafanua anaamini serikali itakubali ombi hilo kwa kuwa imeonesha nia huku akisisitiza uwepo wa nyenzo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 imeonesha jinsi ambavyo sekta binafsi zinavyoweza kuwa mshirika katika utekelezaji wa dira na wao TOL Gases wako tayari.

“Tunafanya uwekezaji mkubwa unaowezesha kuzalisha gesi ya oksijeni kwa ajili ya kuhakikisha kunakuwa na hewa tiba kwa ajili ya mahospitalini hivyo ombi letu Serikali badala ya nayo kuwa inazalisha iweke utaratibu wa kuwa inanunua kutoka sekta binafsi.TOL Gases tunao uwezo mkubwa na tumebobea katika uzalishaji wa oksijeni.”

Kuhusu mkutano wa wanahisa Warungu amesema wamejadili masuala mbalimbali huku akieleza kwa upande wa mapato ya kampuni yaliongezeka kutoka Shilingi bilioni 30.2 mwaka 2024 hadi Shilingi bilioni 31.15 mwaka 2025. 

Amefafanua faida kabla ya riba, kodi, uchakavu na punguzo la thamani (EBITDA) iliongezeka kutoka Shilingi bilioni 10.5 hadi Shilingi bilioni 13.4, huku faida kabla ya kodi ikiongezeka kutoka Shilingi bilioni 3.98 hadi Shilingi bilioni 6.78.”Faida baada ya kodi ilifikia Shilingi bilioni 3.98 mwaka 2025, ikilinganishwa na Shilingi bilioni 2.06 mwaka 2024.”

Ameongeza TOL Gases inaendelea kuongeza uwezo wake wa uzalishaji kupitia miradi miwili mikubwa. Miongoni mwa miradi hiyo ni ujenzi wa kiwanda cha Ikama III cha kuzalisha hewa ya ukaa (Carbon Dioxide), kinachotarajiwa kuanza uzalishaji Septemba 2027. Mradi huo utaongeza uwezo wa uzalishaji na kuimarisha upatikanaji wa gesi hiyo.

Aidha kampuni pia inajenga kituo kipya cha kutenganisha hewa (Air Separation Unit – ASU) kwa msaada wa Clinton Health Access Initiative (CHAI). Kituo hicho kinatarajiwa kuanza kufanya kazi Oktoba 2026 na kitaongeza uwezo wa uzalishaji wa oksijeni hadi takribani tani 20 kwa siku, sambamba na kituo kilichoanza kufanya kazi mwaka 2021.

Warungu amesisitiza uwekezaji huo utasaidia kuongeza ufanisi wa uzalishaji, kurahisisha matengenezo ya mitambo bila kuathiri kwa kiasi kikubwa uzalishaji na kuongeza uwezo wa kukidhi mahitaji ya gesi katika sekta ya afya, viwanda na uzalishaji.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Kampuni hiyo Leonard Kitoka amesema Tanzania kwa sasa ina uwezo wa kutosha kutoka kwa wazalishaji binafsi kukidhi mahitaji ya sasa na yajayo ya oksijeni ya tiba, hasa kutokana na uwekezaji mkubwa uliofanywa hivi karibuni katika mitambo ya uzalishaji.

Akizungumza kuhusu Soko la hisa,amesema  thamani ya hisa za TOL Gases katika Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) imeongezeka kutoka Shilingi 795 wakati wa Mkutano Mkuu wa Mwaka uliopita hadi kufikia kiwango cha juu cha Shilingi 1,490, sawa na ongezeko la takribani asilimia 74. Kwa sasa, hisa hizo zinauzwa kati ya Shilingi 1,320 na Shilingi 1,490.

“TOL Gases imeeleza kuwa rasilimali za umma zinaweza kutumika kwa ufanisi zaidi katika kuongeza mahitaji na upatikanaji wa oksijeni ya tiba badala ya kuwekeza katika kuongeza zaidi uwezo wa uzalishaji.

“Kampuni inapendekeza hospitali na vituo vya afya kuwezeshwa kununua oksijeni yenye ubora unaohakikishwa kutoka kwa wazalishaji binafsi waliopo, hatua ambayo kwa mujibu wa kampuni itasaidia kutumia kikamilifu uwezo wa uzalishaji uliopo nchini, kuepusha uwekezaji unaojirudia na kuhakikisha upatikanaji endelevu wa oksijeni kwa gharama nafuu.”

Amesisitiza TOL Gases  itaendelea kushirikiana na Serikali, taasisi za afya na wadau wa maendeleo kuhakikisha upatikanaji wa oksijeni salama na yenye ubora kwa matumizi ya tiba nchini Tanzania, huku ikiendelea kuwekeza katika uzalishaji, usambazaji na utaalamu wa kiufundi.

Pamoja na hayo amesema kutokana na mikakati ya kampuni hiyo wanahisa kwa kauli moja wamekubaliana kutogawana gawio la faida na badala yake fedha hizo za gawio zitumike katika kuwekeza katika Ujenzi wa miundombinu kwanza ili kuongeza mapato ya kampuni.







Na Mwandishi Wetu

MAMLAKA ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imeteketeza hekari 3,117.9 za mashamba ya bangi na kukamata watuhumiwa 12 katika operesheni maalum ya siku 16 iliyofanyika katika vijiji vinne vya Kata ya Kandawale na Kipatimo, Wilaya ya Kilwa, mkoani Lindi.

Akizungumza kuhusu operesheni hiyo, Kamishna Jenerali wa DCEA, Aretas Lyimo, amesema mafanikio hayo yametokana na ushirikiano mkubwa kati ya Mamlaka, wananchi na viongozi wa maeneo husika katika mapambano dhidi ya kilimo cha bangi.

Amesema operesheni hiyo ni sehemu ya mkakati endelevu wa DCEA wa kudhibiti uzalishaji wa dawa za kulevya nchini hususan bangi, ambayo imeendelea kulimwa katika baadhi ya maeneo nchini.

"Tumebaini uwepo wa mashamba makubwa ya bangi yaliyolimwa katika ardhi zinazomilikiwa na vijiji na vitongoji. Licha ya serikali kuweka mkakati wa matumizi ya ardhi iliyopo chini ya vijiji na vitongoji lakini bado wananchi wanaitumia ardhi hiyo kulima bangi" amesema Lyimo.

Ameeleza kuwa, kati ya wananchi 200 hadi 250 walishiriki kila siku katika kufyeka mashamba hayo, jambo linalodhihirisha umuhimu wa ushiriki wa jamii katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya.

Aidha, ametoa wito kwa wananchi wote wenye mashamba ya bangi au wanaofahamu uwepo wa mashamba hayo katika maeneo yao nchini kuyateketeza mara moja kabla ya hatua za kisheria kuchukuliwa. Vilevile, amewataka viongozi wa vijiji na kata kuhakikisha wanazuia na kutokomeza kilimo cha bangi katika maeneo yao.

Vilevile, amewataka wasimamizi wa hifadhi za taifa na maeneo mengine ya uhifadhi kuhakikisha maeneo wanayosimamia hayatumiki kulima bangi, akisisitiza kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya yeyote atakayebainika kuruhusu au kushindwa kudhibiti shughuli hizo.

Kwa upande wao, wananchi wa Kijiji cha Nandete, Veronica Mandai na Nassoro Mbonde, wamelaani vikali uwepo wa kilimo cha bangi katika maeneo yao, wakisema kuwa hakina manufaa kwa jamii na kimekuwa kikihatarisha mustakabali wa vijana.

Wamesema wakati mwingine watoto wao hujihusisha na kilimo hicho bila wazazi kufahamu, ndiyo sababu wamejitokeza kwa wingi kushiriki katika zoezi la kuteketeza mashamba ya bangi ili kuonyesha msimamo wao wa kupinga kilimo hicho.

"Nawaomba vijana na wanawake wawe mstari wa mbele kukataa na kutokomeza dawa za kulevya kwa sababu zina madhara makubwa kwa afya na maendeleo ya jamii. Vijana ndiyo nguvu kazi ya taifa na wanawajibu wa kulijenga Taifa. Wakijiingiza katika matumizi au uzalishaji wa dawa za kulevya, watapoteza fursa hiyo na kuathiri maendeleo ya taifa. Vilevile, watoto wanaokulia katika mazingira yanayohusisha dawa za kulevya wako katika hatari ya kupoteza mwelekeo wa maisha yao," amesema Veronica.

Naye Afisa Mtendaji wa Kata ya Kandawale, Mohamed Mpame, amesema baada ya operesheni hiyo viongozi wa kata kwa kushirikiana na vijiji na vitongoji wataimarisha ulinzi na usimamizi wa maeneo yao ili kuhakikisha kilimo cha bangi hakiendelei.

"Tutahakikisha tunafanya doria za mara kwa mara na kuendelea kutoa elimu kwa wananchi ili waachane kabisa na kilimo cha bangi ili mwisho wa siku likitokea la kutokea iwe ni juu yao. Nawashauri watu kutumia ardhi yao kulima mazao ya korosho na kuachana na mazao ya bangi” amesema Mpame.

DCEA itaendelea kufanya operesheni nchi nzima kwa kushirikiana na wananchi na wadau mbalimbali ili kubaini na kutokomeza maeneo yote yanayotumika kwa kilimo cha bangi na kuhakikisha hatua stahiki zinachukuliwa kwa mujibu wa sheria.








 

NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo,akizungumza wakati wa Mkutano wa Kati ya Wizara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo,akizungumza wakati wa Mkutano wa Kati ya Wizara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Balozi Waziri Salum,akizungumza wakati wa Mkutano wa Kati ya Wizara ya Viwanda na Biashara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

 Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), Godfrey Nyaisa,akizungumza wakati wa Mkutano wa Kati ya Wizara ya Viwanda na Biashara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

SEHEMU ya washiriki wakimsikiliza Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo (hayupo pichani) ,akizungumza wakati wa Mkutano wa Kati ya Wizara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

SEHEMU ya washiriki wakimsikiliza Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo (hayupo pichani) ,akizungumza wakati wa Mkutano wa Kati ya Wizara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo,akiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kugungua Mkutano wa Kati ya Wizara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo,akiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kugungua Mkutano wa Kati ya Wizara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo,akiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kugungua Mkutano wa Kati ya Wizara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

............

NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo, amewataka Maafisa Biashara nchini kutumia nafasi zao kikamilifu kuibua fursa za uwekezaji, kuongeza thamani ya mazao na kuboresha mazingira ya biashara katika halmashauri, hatua inayolenga kuchochea maendeleo ya kiuchumi na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Londo ametoa kauli hiyo leo Agosti 17,2026 jijini Dodoma  wakati wa Kikao cha Tatu cha Wizara ya Viwanda na Biashara na Maafisa Biashara nchini, kilicholenga kuimarisha utekelezaji wa majukumu yao katika kukuza biashara, viwanda na uwekezaji.

Amesema Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inalenga kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha uchumi wa viwanda katika Afrika Mashariki na Kati, ikiwamo kufikia uchumi wa dola trilioni moja na kuongeza kipato cha Mtanzania hadi dola 7,000. Amesema kufikia malengo hayo kunahitaji uchumi imara, jumuishi na shindani unaotegemea sekta binafsi, sayansi na teknolojia, uwekezaji, utafiti pamoja na nguvu kazi yenye ujuzi.

"Maafisa Biashara wana jukumu la kuhakikisha halmashauri zinakuwa vituo vya uzalishaji, uwekezaji na biashara kwa kutambua fursa zilizopo, kuwaunganisha wazalishaji na masoko na kuhakikisha mazao yanaongezwa thamani. "amesema Mhe.Londo

Hata hivyo ametolea mfano wa mahindi, amesema wakulima wanapaswa kusaidiwa kuondokana na kuuza mazao ghafi na badala yake kuzalisha bidhaa kama unga wenye chapa na kuufikisha kwenye masoko, hatua itakayoongeza kipato na kuchangia kupunguza umaskini.

Aidha, amesema utekelezaji wa Dira 2050 unahitaji vijana, wanawake na watu wenye ulemavu kushirikishwa kikamilifu katika uzalishaji, uwekezaji na biashara kupitia fursa za mikopo na uwezeshaji. Amesema katika mwaka wa fedha 2025/2026, viwanda vikubwa vipya 25 vilijengwa katika sekta mbalimbali na kutoa ajira 39,000, zikiwamo ajira 7,600 za moja kwa moja na 31,000 zisizo za moja kwa moja.

Katika kuimarisha mazingira ya uwekezaji, Londo amezitaka mikoa kuhuisha kanzidata za viwanda, biashara, masoko, leseni, wawekezaji na maeneo yaliyotengwa kwa shughuli za kiuchumi, huku kila halmashauri ikiandaa wasifu wa fursa za uwekezaji unaoonyesha upatikanaji wa malighafi, miundombinu, masoko na maeneo ya uwekezaji. Pia amewataka Maafisa Biashara kuhakikisha Mabaraza ya Biashara yanafanya kazi kikamilifu na hoja za sekta binafsi zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati.

Katika hatua nyingine, Londo amewataka Maafisa Biashara kuharakisha urasimishaji wa biashara zisizo rasmi kwa kutoa elimu kuhusu usajili wa biashara, leseni, TIN, viwango, vipimo na taarifa za umiliki.

Amesema urasimishaji utawawezesha wafanyabiashara kupata huduma za uwezeshaji, mitaji na masoko, huku akieleza kuwa halmashauri zimetengewa asilimia tano ya mapato ya ndani, yenye thamani ya zaidi ya Sh bilioni 72 kwa mwaka wa fedha 2026/2027, kwa ajili ya kuwekeza katika miundombinu ya masoko, maeneo ya biashara na ujasiriamali.

Amesisitiza fedha hizo zitumike kwa ufanisi kwa kushirikisha sekta za ardhi, maji, nishati na barabara ili kuongeza tija kwa wafanyabiashara na kuvutia wawekezaji. Aidha, amewataka Maafisa Biashara kutumia nafasi zao kuboresha huduma na kuifanya Tanzania kuwa na mazingira bora zaidi ya biashara na uwekezaji, hatua ambayo ni muhimu katika kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Balozi Waziri Salum, amewataka Maafisa Biashara kuongeza udhibiti wa bidhaa feki na viwanda visivyo rasmi katika maeneo yao, akieleza kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kulinda afya na usalama wa wananchi, watumiaji pamoja na wazalishaji wanaofuata sheria.

Naye Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), Godfrey Nyaisa, amesema Maafisa Biashara ni kiungo muhimu kati ya Serikali na wafanyabiashara katika kuhakikisha sera, sheria na kanuni za biashara zinatekelezwa na kuleta mabadiliko chanya katika mazingira ya biashara na uwekezaji nchini.

Amesema kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, BRELA imeendelea kuboresha mifumo na sheria zinazosimamia usajili na utoaji wa leseni kwa lengo la kupunguza muda na gharama za kuanzisha na kuendesha biashara. Amesema kupitia BRELA Online System (ORS), huduma za wakala zimeunganishwa katika mfumo mmoja, huku mfumo huo ukiwezesha pia utoaji na usimamizi wa leseni za biashara kundi A na B.

Amesema mfumo huo unatoa fursa kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa kutoa na kusimamia leseni za kundi B bila kuathiri mapato yao, kwani malipo yanayofanywa na mfanyabiashara yanaingia moja kwa moja katika akaunti ya halmashauri husika.

Aidha, ORS imeunganishwa na mifumo ya taasisi nyingine za Serikali ikiwamo NIDA na TRA, hatua inayowezesha taarifa muhimu kupatikana moja kwa moja bila mfanyabiashara kuwasilisha nyaraka ambazo tayari zipo kwenye mifumo hiyo.

Nyaisa,amesema kuwa  maboresho hayo yameongeza uwazi na ufanisi, kupunguza urudufu wa taarifa, muda na gharama za kupata huduma, pamoja na kupunguza mianya ya uzembe katika utoaji wa huduma.

"BRELA itaendelea kushirikiana na Wizara ya Viwanda na Biashara, Ofisi ya Waziri Mkuu–TAMISEMI, sekretarieti za mikoa na halmashauri katika kuwajengea uwezo Maafisa Biashara."amesema Nyaisa

Amesema katika mwaka wa fedha 2026/2027, BRELA imepanga kutoa mafunzo kwa Maafisa Biashara wote nchini kupitia kanda nne, yatakayolenga matumizi ya mifumo, utoaji na usimamizi wa leseni pamoja na utekelezaji wa sheria.

Pia amesema BRELA itaendelea kuboresha miunganiko ya mifumo ya kidijitali na kushirikiana na vyama vya Maafisa Biashara katika kutatua changamoto zao, huku akisisitiza kuwa maafisa hao ni mawakala muhimu wa uwekezaji nchini na wanapaswa kutambua kuwa jukumu lao ni kuwezesha biashara, si kuikwamisha, ili kujenga mazingira rafiki kwa wafanyabiashara na wawekezaji.


Top News