Serikali imevitaka vyama vya wafanyakazi nchini, ikiwemo Chama cha Walimu Tanzania (CWT), kutumia meza ya majadiliano (Social Dialogue) kutatua kero za wafanyakazi badala ya  migongano isiyo na tija inayodhoofisha mshikamano na kushusha morali ya kazi.

Rai hiyo imetolewa na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi,Ajira na Mahusiano Mheshimiwa Dr. Evaline Munisi wakati akifungua rasmi mafunzo ya siku mbili kwa watumishi wa Makao Makuu na Makatibu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT) wa Mikoa na Wilaya kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi hiyo Deus Sangu leo Agosti 13, 2026 mjini Morogoro.

Amesema kuwa Vyama vya Wafanyakazi havikuundwa kwa ajili ya kusigana na Waajiri, bali viliundwa kama jukwaa la kisheria la kukaa meza moja na waajiri ili kujadiliana kwa hoja, ushahidi na kuheshimiana.

"Vyama vya wafanyakazi havikuundwa kwa ajili ya kusigana na waajiri, bali viliundwa kama jukwaa la kisheria la kukaa meza moja ili kupata suluhu ya pamoja. Katika miaka ya hivi karibuni tumeona kuibuka kwa makundi yanayojielekeza zaidi katika propaganda na migongano, jambo linalodhoofisha mshikamano wa walimu na kuathiri ubora wa elimu," alisema.

Akiangazia kaulimbiu ya CWT inayosema "Wajibu na Haki, Naibu Waziri amesema kuwa  mambo hayo mawili ni kama ndugu pacha wanaotembea pamoja, hivyo ni lazima walimu watimize wajibu wao wa kiutumishi kabla ya kudai haki zao.

Amesema ni wajibu wa chama hicho kutetea maslahi ya walimu kama mishahara, upandaji vyeo na malimbikizo, lakini pia ni wajibu wao kuwasimamia walimu wafundishe kwa juhudi na nidhamu.

"Mwalimu asiyetimiza wajibu wake, anayetoroka kazini au anayekiuka maadili anakosa halali ya kimaadili ya kudai haki zake na anakiharibia chama sifa njema. Utendaji bora darasani ndio unaoipa CWT nguvu ya kusimama mbele ya Serikali kudai haki," alisema.

Ameongeza kuwa ulimwengu wa leo unaendeshwa na mifumo ya kidijitali na sheria, hivyo mtazamo wa zamani wa kuendesha vyama kwa mazoea na mihemko hauna nafasi tena, Serikali inatarajia kuona mabadiliko makubwa katika kasi ya kutatua kero za walimu na uadilifu wa matumizi ya fedha baada ya mafunzo hayo.

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri amesema kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kufanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya elimu kwa kujenga miundombinu na kuajiri walimu wapya ili kupunguza mzigo wa kazi.

Aidha Serikali itaendelea kuweka mazingira bora ya kazi na kushirikiana na CWT ili kulinda amani na utulivu mahali pa kazi. Mafunzo hayo ya siku mbili yamejumuisha washiriki takriban 240 yakilenga kuwajengea uwezo katika sheria za kazi, taratibu za Tume ya Utumishi wa Walimu (TSC), na utendaji wa Bodi ya Kitaaluma ya Walimu.

Aikizungumza awali mwakilishi wa Msajili wa Vyama vya Wafanyakazi na Waajiri Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano Mussa Msami amesema kuwa kitengo cah Msajili wa Vyama vya Wafanyakazi na Waajiri milango iko wazi kwa ushauri ushirikiano wakati wote. 






Na Belinda Joseph-Dodoma.

Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Mkoa wa Dodoma limefanya kikao kikao kazi na Maafisa wa Jeshi la Polisi ngazi ya kata, wilaya na Mkoa wa Dodoma, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano katika ulinzi wa miundombinu ya umeme na kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kulinda miundombinu hiyo.

Akizungumza katika kikao hicho, Kaimu Meneja wa TANESCO Mkoa wa Dodoma, Mhandisi Kurwa Mangara, amesema ushirikishwaji wa vyombo vya ulinzi ni muhimu kutokana na nafasi ya umeme katika maisha ya wananchi na shughuli za kiuchumi.

Amesema hatua hiyo imechukuliwa kutokana na changamoto za uhujumu na uharibifu wa miundombinu ya uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa umeme, ikiwemo wizi wa vyuma na bolti pamoja na uvamizi wa maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya njia za kusafirisha umeme.

Mangara ameeleza kuwa baadhi ya maeneo hayo yamekuwa yakitumika kwa shughuli za kilimo na uchimbaji wa mchanga na kokoto, hali inayoweza kusababisha mmomonyoko wa udongo na kuhatarisha nguzo pamoja na miundombinu mingine ya umeme.

Aidha, ametaja changamoto ya kuibiwa nyaya zinazotumika kulinda transfoma na kuchomwa kwa nguzo za umeme wakati wa uandaaji wa mashamba vitendo ambavyo vinaweza kusababisha kukatika kwa umeme, hasara kwa TANESCO na usumbufu kwa wananchi.

Ametoa wito kwa wananchi kutambua thamani ya miundombinu ya umeme na kuacha vitendo vinavyoweza kuhatarisha upatikanaji wa nishati hiyo, akisisitiza kuwa ulinzi wa miundombinu ya umeme ni jukumu la pamoja kwa TANESCO, vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na wananchi.

Kwa upande wake, Kaimu Afisa wa Jeshi la  Polisi  ASP Regina Mtana, amewashukuru TANESCO kwa kutoa elimu hiyo na kuahidi kuwa Jeshi la Polisi litaendelea kushirikiana na shirika hilo katika kuimarisha ulinzi wa miundombinu ya umeme na kuchukua hatua dhidi ya vitendo vinavyoweza kuhatarisha usalama na upatikanaji wa nishati hiyo.





Na Mwandishi Wetu, Dar

Waziri wa Ujenzi, Mhe. Abdallah Ulega (Mb.) amefurahishwa na Huduma zinazotolewa na Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) hususan matumizi ya Moduli ya kupokea na kushughulukia malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST. 

Waziri Ulega ameipongeza PPAA alipotembelea banda la Mamlaka hiyo pembezoni mwa Mkutano wa Mashauriano na Wadau wa Sekta ya Ujenzi kwa Mwaka 2026 unaofanyika tarehe 13 – 14, Agosti, 2026 Jijini Dar es Salaam. 

PPAA imeshiriki maaonesho hayo kwa lengo la kutoa elimu juu ya huduma mbalimbali inazozitoa kwa wadau wa ununuzi wa umma hususan matumizi ya Moduli ya kupokea na kushughulukia malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST. 

Hongereni kwa kazi nzuri ya kutoa elimu kwa wadau wenu hasa wakandarasi walioshiriki katika mkutano wa leo, endeleeni kufanya kazi hii nzuri ili kutimiza azma ya Serikali ya kuwasogezea wananchi huduma kwa karibu zaidi,” amesema Mhe. Ulega 
Kwa Upande wake Mkuu wa Sehemu ya Huduma za Sheria PPAA, Bi. Agnes Sayi ambaye alimwakilisha Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando alimweleza Waziri Ulega kuwa kuanza kwa matumizi ya Moduli ya kupokea malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST kumechangia kuongeza uwazi, uwajibikaji na ufanisi kwenye mnyororo wa ununuzi na ugavi. 

“Mhe. Waziri matumizi ya moduli katika mnyororo wa ununuzi na ugavi yamechangia kutoa maamuzi kwa haki na wakati na kuwezesha miradi ya Serikali kutekelezwa kwa wakati,” amesema Bi. Sayi

Pamoja na mambo mengine, Bi. Sayi amemweleza Mhe. Ulega kuwa  kwa sasa PPAA inatoa huduma ya Mkutano kwa njia ya Mtandao “Video Conference” ambapo hutumika kusikiliza mashauri ya wazabuni walioshindwa kufika katika Ofisi za Mamlaka ya Rufani kwa ajili ya kusikiliza rufaa zilizowasilishwa.

“Huduma ya ‘video conference’ inatoa fursa ya kuwasikiliza wazabuni walioshindwa kufika PPAA na hivyo kuiwezesha Mamlaka ya Rufani kutekeleza jukumu lake la msingi la utatuzi wa migogoro itokanayo na michakato ya ununuzi wa Umma kwa haki na wakati,” ameongeza Bi. Sayi

Awali akifungua Mkutano wa Mashauriano na Wadau wa Sekta ya Ujenzi kwa Mwaka 2026 unaoendelea Jijini Dar es Salaam, Waziri Ulega amewataka Wakandarasi wazawa na wakandarasi wote nchini kwa ujumla kuhakikisha kuwa wanatekeleza miradi wanayoipata kwa weledi na ufanisi.

Aidha, Waziri Ulega ameongeza Serikali imeandaa mikakati ya kuwasaidia Wakandarasi wazawa na Washauri Elekezi ili waweze kunufaika kupitia miradi inayotolewa nchini na kuwataka watendaji wa Wizara ya Ujenzi kutoa ushirikiano na kuhakikisha wanatatua changamoto zinazowakwamisha wakandarasi wa ndani kupata miradi.

Mkutano wa Mashauriano na Wadau wa Sekta ya Ujenzi, umeongozwa na Kaulimbiu, “Dira 2025: Fursaa na Wajibu wa Makandarasi katika ujenzi wa Miundombinu Endelevu”


 

NA DENIS MLOWE IRINGA

MKUU wa Mkoa wa Iringa, Kheri James, amezindua Kliniki ya Watumishi wa Umma inayolenga kusikiliza na kutatua kero zinazowakabili watumishi na wastaafu katika Mkoa wa Iringa, akisisitiza kuwa utatuzi wa changamoto za watumishi ni msingi wa kuboresha huduma zinazotolewa kwa wananchi.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kliniki hiyo uliofanyika katika viwanja vya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Kheri amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuboresha mazingira ya kazi kwa watumishi wa umma kupitia maboresho ya mishahara, upandishaji wa madaraja, ajira mpya na kuimarisha mifumo ya usimamizi wa rasilimali watu.

Alisema pamoja na hatua hizo, bado zipo changamoto zinazowakabili baadhi ya watumishi na wastaafu, ikiwemo malimbikizo ya mishahara, madai ya likizo, uhamisho, matibabu, kupandishwa madaraja, mafao ya wastaafu pamoja na fidia kwa watumishi wanaoumia kazini.

“Lengo la kliniki hii siyo kutafuta makosa ya watu, bali kutafuta suluhisho la madai, manung’uniko na changamoto za watumishi na wastaafu ili wafanye kazi wakiwa na utulivu wa akili, motisha na imani kuwa haki zao zinapatikana pale inapostahili,” alisema Kheri.

Amesema kliniki hiyo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuwafikia watumishi walipo badala ya kuwalazimisha kutumia muda na fedha kusafiri kwenda maeneo mbalimbali kufuatilia changamoto ambazo zinaweza kutatuliwa ndani ya mkoa.

Kheri alisema kuwa mpango huo ni muhimu hasa kwa watumishi wanaotoa huduma za moja kwa moja kwa wananchi, wakiwemo madaktari, walimu na watumishi wengine, ambao wanapokuwa na changamoto zisizotatuliwa wanaweza kushindwa kufanya kazi kwa ufanisi unaotarajiwa.

“Tunataka watumishi wetu wafanye kazi wakiwa na furaha na utulivu tunatatua changamoto za watu wetu ili nao wakaweze kutatua changamoto za wananchi wenzao,” amesema.

Ameongeza kuwa kliniki hiyo itasaidia pia kupunguza muda na gharama ambazo watumishi wamekuwa wakitumia kufuatilia masuala yao katika taasisi za Serikali zilizopo nje ya mkoa

“Yawezekana mwalimu ana jambo linaloweza kushughulikiwa na Ofisi ya Utumishi ya Mkoa au Wilaya, lakini akalazimika kusafiri hadi TAMISEMI au Utumishi hivyo hii kliniki inarahisisha jambo hilo kushughulikiwa hapa hapa Iringa,” amesema.

Kheri pia amewataka viongozi na wataalamu wanaoshiriki katika kliniki hiyo kutoa huduma kwa weledi, uadilifu na heshima, kusikiliza kila mtumishi na mstaafu bila ubaguzi na kutoa majibu yanayozingatia sheria, kanuni na miongozo ya Serikali.

Amesisitiza kuwa pale ambapo suala haliwezi kutatuliwa papo hapo, mtumishi apewe mrejesho wa hatua zitakazochukuliwa pamoja na muda wa utekelezaji, huku akitaka hakuna changamoto inayopuuzwa au kuachwa bila kufuatiliwa.

Aidha amesema ustawi wa watumishi unapaswa kwenda sambamba na ustawi wa wananchi, akieleza kuwa Serikali inapoboresha mishahara, madaraja na mazingira ya kazi, watumishi nao wanapaswa kulipa kwa kutoa huduma bora kwa wananchi.

“Serikali imeshughulika na madaraja, mishahara na maeneo mazuri ya kufanya kazi sisi jitihada hiyo inayofanywa na Serikali lazima tuitafsiri kwa huduma bora kwa wananchi. Ustawi wa watumishi uende sambamba na ustawi wa wananchi,” amesema Kheri.
Kliniki hiyo inafanyika kuanzia Agosti 13 hadi 20, 2026, katika halmashauri zote tano za Mkoa wa Iringa, ambapo watumishi na wastaafu watapata fursa ya kuwasilisha changamoto zao na kupata ufumbuzi au maelekezo ya namna ya kuzifanyia kazi.

Kwa upande wake, Nuru Sobela, ambaye ni mratibu wa Kliniki ya Watumishi wa Umma Mkoa wa Iringa na Katibu Tawala Msaidizi anayeshughulikia masuala ya Utumishi na Usimamizi wa Rasilimali Watu, amesema kliniki hiyo imeandaliwa kwa ajili ya kusikiliza kero na changamoto mbalimbali zinazowakabili watumishi wa umma.

Amesema katika kliniki hiyo yameandaliwa madawati mbalimbali, ikiwemo dawati la mfumo, mishahara, masuala ya watumishi wanaoumia kazini pamoja na dawati maalum kwa ajili ya wastaafu.

Ameeleza kuwa dawati la wastaafu linafanya kazi kwa kushirikiana na PSSSF ili kuhakikisha changamoto za wastaafu zinapatiwa ufumbuzi.
Mbali na masuala ya utumishi, amesema taasisi mbalimbali zimeungana na zoezi hilo kutoa huduma kwa watumishi, zikiwemo NHIF, NIDA na taasisi za benki.

Nuru amewataka watumishi wote wa umma katika Mkoa wa Iringa kutumia fursa hiyo kufikisha changamoto zao ili zipatiwe ufumbuzi kwa wakati.

Amesema baada ya uzinduzi wa kliniki hiyo katika makao makuu ya mkoa, zoezi litaendelea katika maeneo mengine, ambapo tarehe 17 na 18 Agosti litafanyika Wilaya ya Kilolo, huku tarehe 19 na 20 Agosti likifanyika Wilaya ya Mufindi.

Amesema dhamira ya Serikali ni kuhakikisha mtumishi anapata mazingira rafiki ya kuwasilisha hoja zake, kufuatilia haki zake na kupata majibu bila kutumia gharama kubwa au muda mwingi wa kuacha kituo chake cha kazi.





Na Janeth Raphael - MichuziTv

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, amezitaka Kamati za Ushauri wa Stadi (TACs) za Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) kuhakikisha mafunzo yanayotolewa yanaendana na mahitaji halisi ya soko la ajira, teknolojia na mabadiliko ya sekta mbalimbali. Prof. Mkenda amesema mafunzo ya ufundi stadi hayapaswi kuishia katika utoaji wa vyeti, bali yanapaswa kumwandaa mhitimu kuwa na ujuzi, umahiri, ubunifu, nidhamu ya kazi na uwezo wa kutumia teknolojia katika kufanya kazi na kujiajiri.

Akizungumza leo Agosti 13, 2026, jijini Dodoma wakati wa uzinduzi wa Kamati hizo, Prof. Mkenda amesema TACs zinapaswa kuwa “macho na masikio” ya VETA kwa kufuatilia mabadiliko ya teknolojia, uzalishaji na mahitaji ya waajiri katika maeneo ya kazi. Amesisitiza kuwa kamati hizo zisibaki kuwa za mikutano pekee, bali ziwe za matokeo kwa kutoa ushauri wa wakati kuhusu maboresho ya mitaala, kuanzishwa kwa stadi mpya na kuondolewa kwa teknolojia zilizopitwa na wakati.

Waziri Mkenda amesema ushauri wa TACs ni muhimu katika kuhakikisha vijana wanaohitimu wanakuwa na ujuzi unaohitajika na waajiri, huku VETA ikipata fursa ya kuanzisha programu mpya katika sekta zenye fursa za ajira na kujiajiri, ikiwemo TEHAMA, utalii, ukarimu, sanaa, ujenzi, nishati, kilimo na uzalishaji. Amesema waajiri wanapaswa kuwa sehemu ya mfumo wa mafunzo kwa kueleza mahitaji yao ya ujuzi, vifaa, teknolojia na viwango vya utendaji vinavyohitajika.

Akihusisha hatua hiyo na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Prof. Mkenda amesema Tanzania haiwezi kuwa na uchumi imara, jumuishi na shindani bila kuwa na nguvu kazi yenye ujuzi. Amesema elimu na mafunzo ya ufundi stadi ni nyenzo muhimu katika kujenga viwanda vya kisasa, uchumi wa kidijitali na uwezo wa Taifa kuzalisha bidhaa na huduma kwa kutumia maarifa, teknolojia na ubunifu wa ndani.

Aidha, Prof. Mkenda amesema kuanzishwa kwa TACs ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014, Toleo la 2023, inayosisitiza elimu inayokidhi mahitaji ya maendeleo ya Taifa na soko la ajira. Ameeleza pia kuwa Serikali imeendelea kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi za elimu na sekta ya viwanda kupitia Mpango wa Kitaifa wa Ushirikiano kati ya Taasisi za Elimu na Sekta ya Viwanda katika Ukuzaji wa Ujuzi na Uwezeshaji wa Ajira, uliozinduliwa Februari 9, 2026, jijini Dar es Salaam.

Prof. Mkenda amewataka wajumbe wa TACs kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu, weledi, ubunifu, uwajibikaji na uzalendo, huku wakiwa mabalozi wa VETA katika sekta zao na kuhamasisha waajiri kushirikiana na taasisi hiyo katika kuandaa mitaala, kutoa mafunzo kwa vitendo, kuboresha teknolojia na kuandaa nguvu kazi yenye ujuzi unaohitajika. Amesisitiza kuwa utekelezaji wa Dira 2050 hautategemea mipango na nyaraka pekee, bali Watanzania wenye maarifa, ujuzi, ubunifu, nidhamu na uwezo wa kutumia teknolojia.



RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametembelea banda la Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) katika Maonesho yanayoambatana na Tamasha la 10 la Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar.

Katika ziara hiyo, Mhe. Rais Samia amepongeza PSSSF kwa kushiriki katika maonesho hayo na kutoa huduma pamoja na elimu kwa wanachama na wananchi wanaotembelea banda la Mfuko.

Mhe. Rais Samia alipokelewa na Meneja wa PSSSF Ofisi ya Zanzibar, Bi. Mariam Saleh, ambaye alimueleza kuhusu huduma zinazotolewa na Mfuko, pamoja na namna wanachama na wananchi wanavyonufaika na huduma hizo kupitia banda hilo.

Mhe. Rais Samia ameupongeza Mfuko kwa utoaji wa huduma na kusisitiza umuhimu wa kusikiliza na kushughulikia kwa wakati changamoto zinazowasilishwa na wananchi na wanachama.

“Nawapongeza sana kwa huduma nzuri. Kama kuna malalamiko, yakusanyeni na muyafanyie kazi,” ameagiza Mhe. Rais Samia.

Ushiriki wa PSSSF katika Tamasha la Kizimkazi unalenga kuendelea kuwafikia wanachama na wananchi kwa kuwapatia elimu kuhusu hifadhi ya jamii, huduma zinazotolewa na Mfuko pamoja na kuwawezesha kupata ufafanuzi wa masuala mbalimbali yanayohusu mafao na huduma za PSSSF.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Siuluhu Hassan, akizungumza alipotembelea banda la Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) kwenye Maonesho ya Tamasha la Kizimkazi Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar Agosti 12, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kulia), akimsikiliza Meneja wa Ofisi ya Zanzibar ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) Bi. Mariam Saleh, alipotembelea banda la Mfuko huo kwenye Maonesho ya Tamasha la Kizimkazi 2026 (Kizimkazi Festival 2026) Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar Agosti 12, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kushoto), akimsikiliza Meneja wa Ofisi ya Zanzibar ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) Bi. Mariam Saleh, alipotembelea banda la Mfuko huo kwenye Maonesho ya Tamasha la Kizimkazi 2026 (Kizimkazi Festival 2026) Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar Agosti 12, 2026.


 

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe.Salome Makamba,akipata maelezo mara baada ya kutembelea  banda la Mamlaka ya Udhibiti Huduma za Nishati na Maji (EWURA) katika Maonesho ya Kizimkazi yanayoendelea katika Viwanja vya Dimbani, Kizimkazi, Zanzibar.

Na Mwandishi Wetu

Naibu Waziri wa Nishati, Mheshimiwa Salome Makamba, amehimiza umma kupata taarifa sahihi kuhusu hali ya sekta ndogo ya umeme nchini, huku akitoa wito kwa Mamlaka ya Udhibiti Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kuendelea kutoa elimu na taarifa kwa wananchi kuhusu jitihada mbalimbali zinazofanywa na Serikali katika kuboresha huduma za umeme.

Mhe. Makamba ametoa wito huo leo, tarehe 13 Agosti 2026, alipotembelea banda la EWURA katika Maonesho ya Kizimkazi yanayoendelea katika Viwanja vya Dimbani, Kizimkazi, Zanzibar.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, amesema ni muhimu wananchi kupata taarifa sahihi kuhusu kuongezeka kwa uzalishaji na upatikanaji wa umeme nchini na hivyo kukidhi mahitaji tuliyonayo.

“Gharama ya umeme nchini Tanzania ni nafuu ikilinganishwa na nchi jirani, na Serikali inaendelea na juhudi za kuboresha na kuimarisha miundombinu ya umeme ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma hiyo kwa uhakika, hatua itakayochochea maendeleo ya kiuchumi nchini,” aliongeza.

Katika banda la EWURA, Mhe. Makamba alifahamishwa Mamlaka imetumia fursa ya Maonesho hayo kutoa elimu kuhusu masuala mbalimbali ya udhibiti ikiwemo mikataba ya huduma kwa wateja, matumizi sahihi na salama ya huduma za bidhaa za gesi ya mitungi, gesi asilia, umeme na maji, fursa za uwekezaji katika sekta na mengineyo.

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe.Salome Makamba,akisaini kitabu  mara baada ya kutembelea  banda la Mamlaka ya Udhibiti Huduma za Nishati na Maji (EWURA) katika Maonesho ya Kizimkazi yanayoendelea katika Viwanja vya Dimbani, Kizimkazi, Zanzibar.

 

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe.Salome Makamba,akipata maelezo mara baada ya kutembelea  banda la Mamlaka ya Udhibiti Huduma za Nishati na Maji (EWURA) katika Maonesho ya Kizimkazi yanayoendelea katika Viwanja vya Dimbani, Kizimkazi, Zanzibar.


Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Serikali imefanikiwa kupata nafasi nyingine 10 za ufadhili wa masomo kwa wanafunzi wa Kitanzania kupitia mpango wa Samia Scholarship Extended, zitakazowawezesha kwenda nchini Urusi kujiandaa na masomo ya shahada katika Chuo Kikuu cha RUDN, Moscow.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, ameyazungumza hayo leo jijini Dodoma, ambapo amesema nafasi hizo zimetolewa na Chuo Kikuu cha RUDN kufuatia ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, nchini Urusi mwezi Juni 2026, ambapo alifanya mazungumzo na viongozi wa nchi hiyo kuhusu namna ya kuimarisha ushirikiano katika sekta ya elimu.

Kwa mujibu wa Prof. Mkenda, wanafunzi hao 10 wanatarajiwa kuondoka nchini Septemba 1, 2026 na kuelekea Moscow, ambako watashiriki programu maalum ya maandalizi ya masomo maarufu kama bootcamp kwa kipindi cha takribani mwaka mmoja, kabla ya kuanza masomo ya shahada rasmi Septemba 2027.

Ameeleza kuwa wakati wa programu hiyo ya maandalizi, Serikali ya Urusi itagharamia asilimia 80 ya gharama, huku asilimia 20 ikigharamiwa kupitia mpango wa Samia Scholarship Extended. Baada ya wanafunzi hao kuanza masomo yao ya shahada nchini Urusi, Serikali ya Urusi itabeba asilimia 100 ya gharama za masomo yao.

Waziri Mkenda amesema hatua hiyo inaongeza wigo wa fursa za elimu kwa vijana wa Kitanzania, akibainisha kuwa wanafunzi wengine 50 waliopata Samia Scholarship Extended wataenda kusoma nje ya nchi katika maeneo ya Data Science, Artificial Intelligence na Allied Sciences.

Aidha, wanafunzi 1,000 wamepata ufadhili kupitia Samia Scholarship kwa ajili ya kusoma shahada zinazohusiana na sayansi katika vyuo vikuu vya ndani ya Tanzania.

Prof. Mkenda amempongeza na kumshukuru Rais Samia kwa jitihada za kuimarisha mahusiano ya Tanzania na mataifa mbalimbali, akisema nafasi hizo mpya za ufadhili zilizopatikana nchini Urusi zinaonesha mwanzo wa fursa pana zaidi za ushirikiano katika elimu.

Amesema Serikali itaendelea kutumia mahusiano hayo kutafuta fursa zaidi za elimu na ufadhili kwa vijana wa Kitanzania, hususan katika nyanja za sayansi, teknolojia na maeneo mengine yenye umuhimu kwa maendeleo ya taifa.








Na Said Mwishehe, Michuzi TV-Zanzibar

RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, ametoa rai kwa wananchi wa Kizimkazi na maeneo ya jirani, kuilinda na kuitunza miradi yote ya maendeleo iliyozinduliwa na kuwekewa mawe ya msingi, akisisitiza kuwa ni lazima miradi hiyo itunzwe kama mboni za macho.

Dk.Samia aliyasema hayo leo Agosti 13,2026 katika hafla ya uzinduzi wa mradi wa maji Kizimkazi huko katika kiwanja cha Mgombewa katika kijiji cha Kizimkazi Mkunguni ikiwa ni shamra shamra za Tamasha la Kizimkazi 2026.

Amesema, miradi hiyo mikubwa si mali ya serikali pekee, bali ni uhai, fursa, uchumi na ustawi wa maisha ya wananchi wenyewe na kuongeza Serikali inatumia fedha nyingi pamoja na utaalamu mkubwa kuwaletea wananchi maendeleo hivyo ni wajibu wa kila mwananchi kuwa mlinzi wa mwenzake ili kuzuia uharibifu wa miundombinu hiyo.

“Tutunze itufae leo na litufae tena, tuwe walinzi sisi wenyewe kwa wenyewe, tulindane kutokuharibu miundombinu hii,” amesema Rais Samia na kuongeza kukamilika kwa mradi huo mkubwa wa maji utaondoa kero ya muda mrefu kwa wananchi wa Kizimkazi iliyodumu kwa miongo kadhaa.

Dk.Samia alieleza kuwa tangu mwaka 1974, Kizimkazi ilikuwa ikitegemea tangi lenye uwezo wa kuhifadhi lita 150,000 za maji.

Ameeeleza kwa miaka iliyofuata mahitaji ya maji yaliongezeka kutokana na kukua kwa idadi ya watu, maendeleo ya makazi, shughuli za kiuchumi pamoja na uwekezaji katika eneo hilo.

Ameongeza tangi hilo ambalo awali lilitosheleza mahitaji ya wananchi, lakini baadae lilichakaa na kushindwa kukidhi mahitaji yaliyokuwa yakiongezeka siku hadi siku.

Dk.Samia amebainisha kuwa hali hiyo ndiyo iliyosababisha changamoto ya maji kuendelea kuwa miongoni mwa kero kubwa kwa wananchi wa Kizimkazi.

“Sasa hali hii imebadilika baada ya kukamilika na kuzinduliwa kwa mradi mpya wa maji wenye uwezo mkubwa zaidi wa kuhudumia wananchi.Mradi huu umejengwa kwa kuzingatia mahitaji ya sasa na ongezeko la mahitaji ya baadaye.Uwezo wake ukiwa mara mbili ya mahitaji ya sasa ya eneo hilo.”

Ameongeza hatua hiyo haitasaidia Kizimkazi pekee, bali inalenga kuhakikisha huduma ya maji inaendelea kuvuka mipaka na kuwafikia wananchi wa maeneo ya Dimani na Mtende.

Aidha amesema Serikali ina mpango mkubwa zaidi wa kujenga mfumo wa maji wa wilaya nzima, unaojulikana kama district grid, hatua ambayo itapanua zaidi mtandao wa huduma ya maji na kuhakikisha maeneo mengi yanaunganishwa katika mfumo mmoja wa uhakika.

Ameongeza fedha kwa ajili ya utekelezaji wa mpango huo tayari zimepatikana na utekelezaji wake unaanza mara moja.”Kwa Kizimkazi mradi huu haukuwa tu uzinduzi wa miundombinu mipya, bali ni mwanzo wa safari mpya ya huduma ya maji yenye uwezo wa kwenda sambamba na kasi ya maendeleo ya eneo hilo.

Aidha amewataka wananchi kuulinda mradi huo na kueleza Serikali imetumia fedha nyingi kuhakikisha huduma hiyo inawafikia wananchi, hivyo uharibifu wa miundombinu hiyo ni sawa na kuharibu uwekezaji ambao umelenga kuboresha maisha yao wenyewe.

Awali Dk.Samia ametembelea hospital ya Kizimkazi ambapo alipanda mti na kukabidhi gari ya kubebea wagonjwa, ambapo gari hilo limetolewa kwa msaada wa Shirika la Afya Duniani (WHO), ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha huduma za afya kwa wananchi wa eneo hilo.

Rais Samia amesema hospitali hiyo sasa imepiga hatua kubwa katika utoaji wa huduma, ikiwemo kuanza kutoa huduma ya kusafisha damu, dialysis, kwa wagonjwa wenye matatizo ya figo.

Amesisitiza huduma hiyo ni muhimu kwa sababu kwa kawaida huduma za aina hiyo zimekuwa zikipatikana zaidi katika hospitali kubwa zenye huduma za kibingwa.






 

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amemjulia hali, Mama Fatma Karume,Mjane wa Rais wa Kwanza wa Zanzibar Hayati Sheikh Abeid Amani Karume, ambaye anapatiwa matibabu katika Hospitali ya Lumumba Zanzibar. Tarehe 13 Agosti 2026.

Kizimkazi, Zanzibar.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametembelea banda la Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) katika Tamasha la Kizimkazi, ambapo alipokelewa na Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Bw. Masha Mshomba.

Pamoja na kutembelea banda la Mfuko, Mhe. Rais alitembelea mabanda mengine ya taasisi na kujionea huduma mbalimbali zinazotolewa.

Mhe. Rais amefurahishwa na kazi nzuri inayofanywa na NSSF hususan katika kuboresha huduma kwa wanachama.

Katika hatua nyingine, NSSF imeendelea kutekeleza wajibu wake kwa jamii katika maeneo ya elimu, afya, michezo, jamii, mahitaji maalum na wadau wa maendeleo. Katika tamasha la Kizimkazi, Mfuko umewajibika kwa jamii kupitia utoaji wa majiko janja (80L Electric Pressure Cooker) yanayotumia umeme kidogo sana wastani wa ‘units’ 2 kwa saa nzima , ni salama na yanajizima yakiivisha ambayo yametolewa kwa shule za sekondari sambamba na kushiriki, pamoja na wadau wengine wa maendeleo, katika Kongamano la Nishati Safi lililofanyika hapa Kizimkazi.

Utoaji wa majiko janja na ushiriki wa Mfuko kwenye Kongamano la Nishati safi ni hatua zinazoonesha dhamira ya NSSF ya kuunga mkono Ajenda ya Kitaifa ya Nishati Safi ya Kupikia, inayolenga kuongeza matumizi ya nishati safi kwa ajili ya kuboresha afya, kulinda mazingira na kuchochea maendeleo endelevu.







\


Na Mwamvua Mwinyi, Chalinze. Agosti 13, 2026

Shule ya Chalinze Modern Islamic ,Mkoani Pwani, inawajengea wanafunzi ujuzi wa vitendo katika fani mbalimbali ikiwemo udaktari, teknolojia ya habari na mawasiliano (ICT), zimamoto pamoja na utengenezaji wa sabuni za maji, ikiwa ni sehemu ya kuwaandaa kujiajiri na kutumia vipaji baada ya masomo.

Akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maendeleo ya shule hiyo, Mwalimu Mkuu Msaidizi, Rashid Stambuli, alisema mpango huo unalenga kuwapa wanafunzi uelewa mpana wa taaluma wanazozisoma, huku wakitumia vipaji vyao kuwa msaada kwa familia na jamii.

Alieleza shule hiyo imekuwa ikitekeleza mtaala kwa kuunganisha masomo ya darasani na vitendo, kwa kuwa wanafunzi wanahitaji kuona na kufanya kile wanachojifunza ili kuongeza uelewa na kuwajengea hamasa ya kusomea taaluma mbalimbali.

“Ni kawaida yetu kufuata mitaala na maagizo yanayotolewa na serikali, mitaala inabadilika na kuboreshwa ambapo watoto wasiwe darasani pekee, bali wanapaswa kutoka kuona na kuamini kwa vitendo,” alifafanua Stambuli.

Alibainisha kuwa, tofauti na baadhi ya shule zinazowapeleka wanafunzi kujifunza kwenye mbuga za wanyama ama maabara, Chalinze Islamic Modern School imeongeza mazingira ya kujifunzia ndani ya shule kwa kuwafundisha wanafunzi kwa kutumia wanyama kama sungura katika kujifunza masuala ya sayansi na udaktari.

“ Tunawaleta wanyama kama sungura shuleni na kuangalia mfumo wa chakula tumboni, Hatuishii hapo, wanafunzi wanaonyeshwa namna ya kufanya huduma mbalimbali za kitabibu kama kuweka drip ,kufunga ogo na matumizi ya oksijeni,” alisisitiza Stambuli. 

Stambuli alisema mpango huo umeanza kuzaa matunda, akieleza kuwa baadhi ya wanafunzi wa kike wameanza kuonyesha umahiri katika masuala ya udaktari tangu wakiwa darasa la sita na sasa wamefikia kidato cha pili.

Alitoa wito kwa wazazi na walezi kutowapangia watoto masomo au taaluma bila kuzingatia vipaji na uwezo wao, akisema malezi yanapaswa pia kuwapa nafasi watoto kukuza vipaji walivyonavyo.

Katika eneo la kukabiliana na majanga ya moto, Stambuli alieleza, shule hiyo ilianza kushirikiana na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kutoa mafunzo kwa wanafunzi na wafanyakazi takribani miaka mitatu iliyopita.

Alisema mafunzo hayo yalionekana kuwa muhimu zaidi baada ya kutokea kwa janga la moto shuleni wiki mbili baada ya kuanza kwa utaratibu huo, ambapo baadhi ya wafanyakazi na wanafunzi waliokuwa wamepata mafunzo waliweza kushiriki katika hatua za awali za kukabiliana na tukio hilo.

“Hii ni taasisi ambayo ina watu zaidi ya 1,000 katika kituo na tunatumia majiko pamoja na umeme, hivyo tahadhari na elimu ya kukabiliana na majanga ya moto ni lazima na elimu hiyo ni endelevu,” anasisitiza Stambuli.

Kwa upande wake, Mkaguzi Msaidizi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji ambaye pia ni Mkuu wa Kituo cha Zimamoto Chalinze, Mariah Gulam Kasekwa, anasema mkakati wa jeshi hilo ni kuhakikisha jamii inapata elimu ya kujikinga na majanga ya moto, ikiwemo kutambua vyanzo vya moto na hatua za kuchukua pindi moto unapotokea.

Kasekwa alisema elimu hiyo ni muhimu zaidi katika maeneo yenye mikusanyiko mikubwa ya watu kama shule, kutokana na uwepo wa wanafunzi na matumizi ya nishati mbalimbali.

Akizungumza kuhusu ndoto yake, mwanafunzi wa kidato cha pili wa Chalinze Islamic Modern School, Shadya Maulid, alisema analenga kuwa daktari na tayari amekuwa akitumia ujuzi anaoupata shuleni kuwasaidia wanafunzi wenzake kujifunza masuala ya afya.

“Kwa sasa nafundisha wanafunzi wenzangu wa shule ya msingi akiwemo Haitham Swedi, Aisha Adam, Rahma Ally na Baraka Sharifu. Tunatumia zaidi kufanya vitendo kupitia sungura ambao wanafugwa hapa shuleni,” alieleza Shadya.

Naye mwanafunzi wa darasa la saba, Baraka Sharifu, ambaye amebobea katika mafunzo ya awali ya zimamoto na baadhi ya vitendo vya huduma za afya ikiwemo uwekaji wa drip, aliishukuru serikali kwa kuboresha mitaala na kusaidia upatikanaji wa vifaa vya kufundishia vinavyowawezesha wanafunzi kujifunza kwa vitendo.

Alielezea kwamba, mafunzo hayo yamewajengea wanafunzi ujasiri, uelewa na hamasa ya kuendeleza vipaji vyao katika taaluma mbalimbali.




 


Na Mwandishi Wetu
TEKNOLOJIA na matumizi jumuishi ya mtandao vinaweza kuwa nyenzo muhimu katika kuondoa vikwazo vinavyowakabili watu wenye mahitaji maalum katika elimu, ajira na kujiajiri, wadau wa Internet Governance wamesema.

Akizungumza katika mafunzo ya Tanzania School of Internet Governance, mtaalamu wa masuala ya Ujumuishwaji amesema Profesa Cosmas Mnyanyii watu wenye ulemavu, hususan wasioona na viziwi, bado wanakabiliwa na changamoto kubwa ya kupata ajira katika sekta mbalimbali, hali inayohitaji matumizi zaidi ya teknolojia kuwawezesha kujitegemea.

Amesema tafiti na uzoefu unaonyesha kuwa watu wenye ulemavu mara nyingi hujikuta wakifanya kazi chache zisizohitaji ujuzi mkubwa, hivyo teknolojia inapaswa kutumika kuwapa ujuzi unaowawezesha kushindana katika soko la ajira na kujiajiri.

Kwa mujibu wake, mafunzo ya matumizi ya kompyuta kwa wasioona na viziwi yameonyesha kuwa teknolojia inaweza kuwawezesha kufanya kazi kwa kujitegemea bila kutegemea wasaidizi, akitoa mfano wa watu waliopata mafunzo na sasa wanaweza kwenda kazini na kutekeleza majukumu yao wenyewe.

Amesema Internet Governance ina uhusiano mkubwa na digital inclusion, kwa kuwa usimamizi mzuri wa mtandao unapaswa kuhakikisha makundi yote katika jamii, wakiwemo watu wenye mahitaji maalum, yanapata fursa sawa za kutumia teknolojia na kunufaika na uchumi wa kidijitali.

Aidha, amesema kuna umuhimu wa kuandaa mfumo maalum wa kuwajengea uwezo watu wenye ulemavu, ikiwamo kuwafundisha viziwi kupitia viziwi wenzao na wasioona kupitia wasioona wenzao, hasa katika matumizi ya teknolojia na ujuzi wa kujiajiri.

Amesema hatua hiyo inaweza kusaidia kutatua changamoto zinazotokana na upungufu wa walimu wenye uwezo wa kutumia lugha na mbinu zinazofaa kuwafundisha watu wenye mahitaji maalum, huku ikiongeza idadi ya watu wenye ulemavu wanaoweza kuingia katika sekta za TEHAMA.

Kwa upande wake, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, College of ICT, Dkt.Joseph Mushi amesema chuo hicho kinashirikiana na Tanzania Internet Governance Chapter kuwawezesha vijana kupata ujuzi unaoendana na mahitaji ya dunia ya sasa, ikiwamo kupitia mafunzo na uboreshaji wa mitaala.

Amesema UDSM imekuwa ikifanya mapping kati ya mahitaji yanayotokana na sekta ya TEHAMA na yale yanayojadiliwa kupitia Internet Governance, ili kuhakikisha wahitimu wanakuwa na ujuzi unaoendana na mahitaji ya soko la ajira na fursa za kidijitali.

Naye Mkurugenzi wa Internet Society Tanzania Chapter, Dkt. Nazarius Kirama, amesema Tanzania School of Internet Governance inalenga kuwawezesha wananchi kutoka makundi mbalimbali kuelewa kuwa usimamizi wa Internet si jukumu la mtu mmoja, bali ni suala linalohitaji ushiriki wa Serikali, sekta binafsi, mashirika yasiyo ya kiserikali, wataalamu, vyuo na wananchi.

Amesema elimu ya kidijitali inapaswa kupewa kipaumbele ili wananchi waweze kutumia Internet kama fursa ya elimu, ajira na ujasiriamali, huku akitoa wito kwa Serikali na wadau wengine kushirikiana kuhakikisha digital inclusion inafikiwa katika maeneo yote nchini.


Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewataka wananchi wa Kizimkazi na maeneo jirani kutunza na kulinda miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali, akisisitiza kuwa miradi hiyo ni msingi wa uchumi na ustawi wa wananchi wa sasa na vizazi vijavyo.

Rais Samia ametoa kauli hiyo leo Alhamisi, Agosti 13, 2026, Zanzibar, mara baada ya kuzindua Mradi wa Maji Kizimkazi, ambapo amesema uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali kupitia miradi mbalimbali unapaswa kulindwa ili iendelee kutoa huduma na manufaa yaliyokusudiwa kwa muda mrefu.

“Ni wajibu na ni lazima tutunze miradi hii kama tunavyotunza macho yetu. Miradi hii ni fursa zetu, ni uchumi na ustawi wa maisha yetu,” amesema Rais Samia.

Amesema mafanikio ya utekelezaji wa miradi hiyo yanatokana kwa kiasi kikubwa na uwepo wa amani nchini, hivyo amewataka wananchi kuendelea kuitunza amani ili Serikali iweze kuendelea kutekeleza miradi ya maendeleo na kuboresha maisha yao.

“Miradi hii tumeweka kuileta kwa sababu nchi yetu ina amani. Niombe sana ndugu zangu tuendelee kutunza amani yetu ili tupate maendeleo zaidi,” amesema.

Rais Samia pia amesema kaulimbiu ya “Mapinduzi Daima” inapaswa kuendelea kuakisi mapinduzi katika maendeleo na kuboresha maisha ya wananchi, akieleza kuwa Mapinduzi yalishafanyika na jukumu la sasa ni kuhakikisha mafanikio hayo yanaendelezwa kupitia maendeleo endelevu.

“Tunaposema Mapinduzi Daima, Mapinduzi ya sasa ni maendeleo,” amesema.

Akizungumzia Mradi wa Maji Kizimkazi, Rais Samia amesema mradi huo umejengwa kwa kuzingatia mahitaji ya sasa pamoja na ongezeko la watu na ukuaji wa miji, huku uwezo wake ukiwekwa karibu mara mbili ya mahitaji ya sasa ili kuhakikisha wananchi wanaendelea kupata huduma ya maji hata katika miaka ijayo.

Amesisitiza kuwa wananchi wanapaswa kuupenda, kuutunza na kuilinda miundombinu ya mradi huo kwa kuwa fedha nyingi zimetumika katika utekelezaji wake, hivyo uharibifu au matumizi yasiyo sahihi yanaweza kupunguza au kudhoofisha manufaa yanayotarajiwa.

Rais Samia amesema utunzaji wa miradi ya maendeleo ni jukumu la pamoja kati ya Serikali na wananchi, akisisitiza kuwa kulinda miundombinu hiyo ni kulinda uwekezaji unaolenga kuboresha maisha ya wananchi na kuhakikisha huduma hizo zinaendelea kunufaisha jamii kwa sasa na vizazi vijavyo.





Top News