Na Janeth Raphael - MichuziTv
Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimeendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuimarisha uzalishaji wa mapato ya ndani kwa kuanzisha kampuni ya uwekezaji itakayoratibu na kusimamia vitengo mbalimbali vya uzalishaji visivyo vya kitaaluma, hatua inayolenga kuongeza ufanisi, tija na uwezo wa Chuo kujiendesha kibiashara.
Akizungumza na vyombo vya habari kuhusu mafanikio ya SUA katika kipindi cha Awamu ya Sita, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu hicho, Prof. Raphael Chibunda, amesema SUA kupitia kampuni yake ya uwekezaji ya SUA Income Generation & Services Ltd, inaendelea kutekeleza mikakati madhubuti ya kutumia rasilimali zake katika shughuli zenye uwezo wa kuzalisha mapato na kuchochea maendeleo ya Chuo.
Amesema katika kutekeleza mkakati huo, ukarabati wa majengo ya Kiwanda cha Uchapishaji (Printing Unit) pamoja na Kitengo cha Maziwa (Dairy Unit) umekamilika, huku baadhi ya mitambo ya uchapishaji ikiwa tayari imefungwa na kuwekwa katika hali ya kuanza uzalishaji.
Prof. Chibunda amesema SUA pia inaendelea kutumia mitambo ya Feed Mill & Silos kwa ajili ya uzalishaji wa chakula cha mifugo, kuku na samaki, hatua ambayo pamoja na kusaidia mahitaji ya uzalishaji wa Chuo, inalenga pia kuongeza mapato kupitia shughuli za kibiashara.
Katika kuimarisha uwekezaji wa muda mrefu, amesema SUA imeanza kutumia rasilimali zake za misitu katika fursa za uchumi wa kijani, ambapo Msitu wa Ifinga wenye ukubwa wa hekta 10,000, uliopo Wilaya ya Madaba mkoani Ruvuma, unalengwa kutumika katika biashara ya kimataifa ya hewa ukaa (Carbon Trading).
Amesema tayari hekta 1,500 za msitu huo zimepandwa miti ya biashara, hatua inayoweka msingi wa Chuo kushiriki katika soko la kimataifa la hewa ukaa huku kikihakikisha matumizi endelevu ya rasilimali za misitu.
Aidha, amesema SUA imeendelea kuwekeza katika kilimo cha mazao yenye fursa za kibiashara, ambapo katika Shamba la Biashara lililopo Kampasi ya Solomon Mahlangu, jumla ya ekari 200 za mkonge zimepandwa na ekari 100 za mwanzo tayari zimefikia hatua ya kuanza kuvunwa kwa ajili ya uzalishaji wa nyuzi za katani.
Prof. Chibunda amesema katika kuimarisha usimamizi wa shughuli hizo, mwezi Mei 2026 Baraza la Chuo liliunda Bodi ya Usimamizi na kumteua Meneja wa Mpito wa SUA Income Generation & Services Ltd, kwa ajili ya kuanza utekelezaji wa shughuli za kampuni hiyo.
Amesema kampuni hiyo inatarajiwa kuchukua na kusimamia vitengo vyote vya uzalishaji ambavyo si vya kitaaluma lakini vina uwezo mkubwa wa kuzalisha mapato kwa Chuo, ikiwemo Shamba la Biashara la Kampasi ya Solomon Mahlangu pamoja na vitengo vyake vya maziwa, nguruwe, malisho, shamba na uzalishaji wa chakula cha mifugo.
Vitengo vingine vinavyolengwa kuingia katika uwekezaji huo ni pamoja na Kiwanda cha Samani cha Vuyisile (Vuyisile Mini Furniture Factory) kilichopo Kampasi ya Solomon Mahlangu na SUA Printing Press kilichopo Kampasi ya Edward Moringe.
Kwa upande mwingine, amesema maghala mawili yaliyopo Kampasi ya Solomon Mahlangu yako katika mpango wa ukarabati ili yaweze kutumika kuanzisha kiwanda kidogo cha kuchakata matunda na kuzalisha bidhaa mbalimbali zikiwemo sharubati, maji ya kunywa pamoja na tomato sauce.
Mbali na shughuli hizo, Prof. Chibunda amesema SUA imeendelea kuwekeza katika maeneo mengine ya kimkakati kwa ajili ya kuimarisha shughuli za kitaaluma na kuongeza mapato ya ndani, ikiwa ni pamoja na uzalishaji wa chakula cha samaki na mifugo pamoja na uzalishaji wa matofali kwa ajili ya mafunzo na biashara.
Amesema Chuo pia kinaendelea kupanda miti na kununua vifaa vya kisasa vya kukatia magogo katika eneo lake la Msitu wa Mafunzo wa Olmotonyi jijini Arusha, huku kikiboresha Shamba la Mafunzo la Mfano kwa ajili ya kutoa mafunzo ya vitendo kwa wanafunzi, wakulima na wadau wengine.
Kwa mujibu wa Prof. Chibunda, Shamba hilo pia linatumika kama chanzo cha mapato ya ndani kupitia uzalishaji na uuzaji wa miche, matunda, mbogamboga, maziwa, vifaranga vya samaki na bidhaa nyingine za kilimo. Shamba hilo lina mazao na mifugo inayowakilisha kanda mbalimbali za Tanzania, ikiwemo samaki, ng’ombe, mbuzi, kuku, kondoo, ngamia, farasi na sungura.
Aidha, SUA imeendelea kuboresha miundombinu yake katika maeneo mbalimbali, ikiwemo majengo ya Morning Sight kwa ajili ya shughuli za utalii, pamoja na majengo ya Chuo yaliyopo mjini ambayo yanalengwa kutumika katika shughuli mbalimbali za kuongeza mapato.
Katika sekta ya afya, Prof. Chibunda amesema Chuo kimeendelea kuboresha Hospitali ya SUA kwa kuongeza miundombinu ya kutolea huduma, ikiwemo ujenzi wa wodi za wagonjwa na ununuzi wa vifaa tiba, hatua inayolenga kuongeza uwezo wa hospitali hiyo kutoa huduma bora kwa jamii.
Amesema uwekezaji huo ni sehemu ya mkakati mpana wa SUA wa kutumia ipasavyo rasilimali ilizonazo, kuimarisha shughuli za kitaaluma na uzalishaji, kuongeza vyanzo vya mapato na kujenga uwezo wa Chuo kujiendesha kwa ufanisi zaidi kupitia shughuli za kibiashara na uzalishaji wa ndani.
NA MWANDISHI WETU, DODOMA
Makamu wa Rais, Deogratius Ndejembi, ameelezwa kuwa kiongozi mahiri, muadilifu na mzalendo, mwenye uwezo wa kumsaidia majukumu Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.
Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Taifa, Mary Chatanda, Agosti 30, 2026, ofisini kwake Dodoma, siku moja baada ya kukamilika uapisho wa kiongozi huyo, Ikulu ya Chamwino, Dodoma.
Chatanda ameeleza, Ndejembi ni kiongozi wa vitendo na katika majukumu aliyoaminiwa tangu akiwa Mkuu wa wilaya ya Kongwa, Mbunge, Naibu Waziri na Waziri kamili katika wizara mbalimbali.
"Kule Kongwa Dodoma akiwa Mkuu wa wilaya alifanya kazi nzuri na katika kilimo alisimamia kwa mafanikio makubwa kampeni yake aliyoiita ONJAKO yaani Ondoa Njaa Kongwa. Alihimiza wananchi kulima mazao yanayostahimili ukame kama mtama, mihogo, ufuta na alizeti ili kuwaepusha wananchi na kadhia ya njaa," amesema Chatanda.
Ameongeza kuwa, kampeni ya ONJAKO ilipokelewa vizuri na wakulima wa Kongwa kutokana na mwanzo kutilia mkazo zao la mahindi ambalo mara kwa mara walikuwa wakipata mazao kidogo kutokana na changamoto ya ukame wilayani humo.
Akisisitiza utendaji uliotukuka wa Ndejembi, Chatanda amesema, Wizara kadhaa alizohudumu zikiwemo Tamisemi, Vijana, Ardhi, Nishati, ameacha alama kubwa kwa kuwa mstari wa mbele kutatua changamoto za wananchi.
"Ndejembi si mtu wa kukaa ofisini kusubiri taarifa, anakwenda mwenyewe kujionea utekelezaji wa majukumu na maagizo mbalimbali. Ndiyo maana nasema, Rais Dk. Samia amepata msaidizi mchapakazi na hodari kwelikweli," ameongeza.
Katika hatua nyingine, Mwenyekiti huyo wa UWT Taifa, ametoa rai kwa wananchi kumuombea Rais Dk. Samia, Makamu wa Rais, Ndejembi na viongozi wengine ili waweze kusimamia mipango iliyopo ambayo imejikita katika kukuza ustawi na maendeleo ya wananchi.
Awali, katika uapisho huo, Rais Dk. Samia amemuasa Makamu wa Rais Mteule kuwatumikia Watanzania bila kujali tofauti zao ili kufanikisha utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2025-2030 na Dira ya Maendeleo ya miaka 25 ijayo (2050).
Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Profesa Raphael Chibunda, ameeleza kwa kina historia ya mradi wa mafunzo na utafiti wa panya unaoendeshwa na chuo hicho kwa zaidi ya miaka 25, huku akifichua namna panya shujaa Magawa alivyoweka historia duniani kabla ya kufariki.
Prof. Chibunda amezungumza hayo leo jijini Dodoma katika Mkutano na wanahabari, ambapo amesema mradi huo umekuwa ukifanyika SUA kwa zaidi ya miaka 25, ukiwalenga panya wanaofundishwa kufanya kazi mbalimbali za utafiti na huduma za kijamii, huku akibainisha kuwa panya hao wanaotumika katika mradi huo ni wa asili ya Tanzania.
Kwa mujibu wa Prof. Chibunda, panya hao walitokana na eneo la Milima ya Uluguru mkoani Morogoro, lakini kutokana na kukua kwa mradi huo, SUA kwa sasa ina kituo maalum kinachoshughulikia uzalishaji, malezi na mafunzo ya panya hao.
Amesema mfumo wa malezi na mafunzo ya panya hao umeandaliwa kwa namna ya kipekee chuoni hapo, ambapo kuna maeneo maalum kwa ajili ya panya wanaozalishwa, wanaoanza mafunzo, wanaomaliza mafunzo pamoja na wale wanaostaafu.
“Ukimfika kwetu utakuta tuna wodi ya wazazi, tuna wanaoanza mafunzo, waliohitimu, lakini pia tuna banda la panya wastaafu. Wako pale wanapata pensheni,” amesema Prof. Chibunda.
MAGAWA ALIWEKA HISTORIA CAMBODIA
Akizungumzia panya maarufu duniani Magawa, Prof. Chibunda amesema alikuwa miongoni mwa panya waliopewa mafunzo nchini Tanzania na baadaye kupelekwa Cambodia kwa ajili ya kusaidia kutambua mabomu ya ardhini.
Amesema uamuzi wa kumpeleka Magawa nchini Cambodia ulitokana na ukweli kwamba Tanzania haikuwa na changamoto kubwa ya mabomu ya ardhini kama ilivyokuwa katika baadhi ya maeneo ya nchi hiyo ya Kusini-Mashariki mwa Asia.
Magawa alifanya kazi hiyo kwa mafanikio makubwa na hatimaye kuingia katika historia ya dunia baada ya kugundua idadi kubwa ya mabomu ya ardhini, akivunja rekodi na kuwa miongoni mwa wanyama mashuhuri zaidi waliowahi kutumika katika kazi hiyo.
Uwezo wake wa kugundua mabomu ulimfanya kupata umaarufu mkubwa kimataifa, huku akitunukiwa pia nishani ya heshima kutokana na mchango wake katika kuokoa maisha ya watu na kusaidia kuondoa mabomu hatari yaliyokuwa yamesalia ardhini.
UMRI WA PANYA NA KIFO CHA MAGAWA
Prof. Chibunda amesema panya wanaofundishwa katika mradi huo wana wastani wa maisha wa takribani miaka minane, huku miaka tisa ikiwa ni hatua ya uzee mkubwa kwa panya hao.
Ameeleza kuwa wanapofikia umri huo, huanza kudhoofika kimwili na wanaweza hata kupoteza meno, hali inayowafanya kushindwa kuendelea na shughuli zinazohitaji uwezo mkubwa wa kimwili.
Magawa naye alifikia hatua hiyo ya uzee na hatimaye kufariki dunia akiwa nchini Cambodia, baada ya kutumikia kwa mafanikio katika kazi ya kutambua mabomu ya ardhini.
SUA ILITAKA MAGAWA AREJESHWE TANZANIA
Akijibu swali kuhusu iwapo kulikuwa na mpango wa kumrejesha Magawa nchini Tanzania baada ya kufariki, Prof. Chibunda amesema mpango huo uliwahi kufikiriwa, lakini changamoto za taratibu na vibali vya usafirishaji zilisababisha kutotekelezwa kwa wakati.
“Tunasema ingewezekana, lakini kwa wakati ule taratibu na vibali vya kilojistiki viligoma. Wenzetu kule Cambodia walikosa uvumilivu wa kusubiri, wakamjengea mnara mkubwa kule,” amesema Prof. Chibunda.
Kwa hatua hiyo, Magawa aliendelea kubaki nchini Cambodia ambako alifanya kazi kubwa ya kusaidia kutambua mabomu ya ardhini na kuokoa maisha ya watu.
Historia ya Magawa inaendelea kuwa sehemu muhimu ya mafanikio ya mradi wa SUA wa kufundisha panya kwa matumizi mbalimbali, ikionyesha namna utafiti unaofanywa Tanzania unavyoweza kuzalisha matokeo yenye kutambulika kimataifa.
Mradi huo pia unaendelea kuifanya SUA kuwa miongoni mwa taasisi zinazotumia utafiti na ubunifu katika kutumia uwezo wa wanyama katika kutatua changamoto za kijamii, kiafya na kiusalama.
Na Janeth Raphael - MichuziTv - Bungeni Dodoma.
Serikali imesema imeweka mikakati mbalimbali ya kukuza vipaji na ujuzi kwa vijana wenye ulemavu, kuwawezesha kupata ajira zenye staha na kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi.
Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Dkt. Jafar Seif, wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Yumna Mmanga Omar, lililohusu mkakati mahsusi wa Serikali wa kukuza vipaji na ujuzi kwa vijana wenye ulemavu ili kuongeza ajira na ushiriki wao katika uchumi.
Akijibu swali hilo, Dkt. Seif amesema Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2025–2030, hususan Kifungu cha 95, imeweka msisitizo wa kuwashirikisha na kuwawezesha watu wenye ulemavu kupata ajira zenye staha pamoja na kujenga uwezo wao ili washiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi.
Amesema Serikali pia inatekeleza Mkakati wa Kitaifa wa Kukuza na Kuendeleza Vipaji na Ujuzi kwa Vijana unaoongozwa na Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Vijana ya mwaka 2007, Toleo la mwaka 2024.
Kwa mujibu wa Dkt. Seif, Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 nayo imeweka mkazo katika kukuza elimu jumuishi na kuhakikisha vijana wenye ulemavu wanapata fursa sawa katika elimu, mafunzo ya ufundi, ajira na shughuli mbalimbali za kiuchumi.
Amesema mikakati hiyo inalenga kuhakikisha ulemavu hauwi kikwazo kwa mtu kutumia kipaji, uwezo na ujuzi wake katika kujenga maisha yake na kuchangia maendeleo ya Taifa.
Katika utekelezaji wa mikakati hiyo, Serikali imewezesha vijana wenye ulemavu kupata mafunzo ya ufundi stadi katika maeneo mbalimbali nchini.
Dkt. Seif amesema jumla ya vijana 643 wenye ulemavu walijiunga na kuhitimu mafunzo ya ufundi stadi katika vyuo vitano, vikiwemo vya VETA, katika kipindi cha mwaka 2023 hadi 2025.
Amesema vijana hao walipata ujuzi katika fani mbalimbali zikiwemo umeme wa majumbani, useremala, uungaji vyuma, ushonaji wa nguo na viatu, kilimo na ufugaji, pamoja na ujenzi na uashi.
Mbali na mafunzo, Serikali imeendelea kuweka mazingira ya kuwawezesha vijana wenye ulemavu kutumia ujuzi walioupata katika kujiajiri na kushiriki katika uchumi.
Dkt. Seif amesema Serikali imetenga asilimia 30 ya zabuni za umma kwa ajili ya kuwawezesha makundi yanayolengwa, ambapo hadi mwaka 2024/25 jumla ya vikundi 703 vya watu wenye ulemavu vilikuwa vimesajiliwa katika mfumo wa NeST.
Hatua hiyo inalenga kuhakikisha kuwa ujuzi na vipaji vinavyopatikana kupitia mafunzo vinaweza kugeuzwa kuwa fursa za ajira, ujasiriamali na kujikwamua kiuchumi.
Aidha, Serikali imeendelea kutenga asilimia 10 ya mapato ya Halmashauri kwa ajili ya mikopo kwa makundi maalum, ambapo asilimia mbili hutengwa kwa ajili ya watu wenye ulemavu.
Katika kipindi cha mwaka 2021 hadi 2026, Serikali imesema jumla ya Shilingi bilioni 26.87 zimetolewa kwa ajili ya kuwawezesha watu wenye ulemavu kupitia mikopo hiyo.
Serikali imesisitiza kuwa hatua hizo ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha vijana wenye ulemavu wanapata fursa sawa za kujenga vipaji, kupata ujuzi, kuajiriwa au kujiajiri na hatimaye kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii ya Taifa.
Baraza la Masoko ya Mitaji linatarajia kuimarisha ushirikiano kwa kubadilishana uzoefu katika usimamizi wa kesi, utatuzi wa migogoro na matumizi ya teknolojia, huku shughuli za biashara na uwekezaji nchini zikiendelea kukua.
Ushirikiano huo utaliwezesha baraza la masoko ya mitaji ambalo ni baraza jipya, kujifunza kutokana na uzoefu wa baraza la ushindani ambalo tangu lilipoanza kusikiliza migogoro mwaka 2007, limewahi kushughulikia zaidi ya kesi 525.
Maofisa wa taasisi hizo walijadili ushirikiano huo wakati ujumbe wa baraza la masoko ya mitaji ulipotembelea baraza la ushindani.
Akizungumza kuhusu ushirikiano huo Msajili wa baraza la ushindani Mbegu Kaskasi, alisema pia kubadilishana uzoefu kutasaidia taasisi hizo kuboresha huduma na kuhakikisha migogoro inayohusu wafanyabiashara na wawekezaji inatatuliwa ndani ya muda unaofaa.
“Tumekuwa hapa kwa karibu miaka 20. Wao wamekuja kujifunza kutokana na uzoefu wetu, lakini sisi pia tumejifunza mengi kutoka kwao licha ya kuwa wameanzishwa miaka mitatu iliyopita,” alisema.
Kaskasi alisema baraza hilo hushughulikia wastani wa kesi 45 hadi 50 kwa mwaka, zikiwamo zinazohusu bidhaa bandia na migogoro inayotokana na maamuzi ya mamlaka za udhibiti.
Alisema uzoefu huo unaweza kusaidia baraza la masoko ya mitaji kujenga mifumo bora ya usimamizi wa kesi kadri idadi ya wawekezaji na wafanyabiashara inavyoongezeka.
Kaskasi alisema utatuzi wa migogoro kwa haraka ni muhimu kwa sababu kesi zinazochukua muda mrefu zinaweza kuathiri thamani ya bidhaa na mali za kifedha.
“Ikiwa bidhaa zinashikiliwa kwa miaka miwili, zinaweza kuharibika. Kwa upande wa fedha, kama fedha zimefungwa na haziwezi kutumika kwa miaka miwili, thamani yake hupungua. Katika sekta ya fedha, muda ni kila kitu,” alisema.
Alisema lengo kuu la mabaraza hayo ni kuwezesha shughuli za biashara na kujenga mazingira bora zaidi kwa wawekezaji.
“Lengo la mabaraza haya ni kuchochea maendeleo ya nchi, kurahisisha biashara na kuvutia wawekezaji,” alisema.
Kwa upande wake, Msajili wa baraza la masoko ya mitaji Dk Martin Kolikoli, alisema taasisi hiyo ina nia ya kujifunza zaidi namna baraza la ushindani inavyopanga na kuratibu kesi ili kuhakikisha maamuzi yanatolewa kwa wakati.
baraza la masoko ya mitaji limekuwa likifanya kazi kwa takribani miaka mitatu na hadi sasa limesajili migogoro sita. Kesi mbili zilirudishwa kutokana na changamoto za kiutaratibu, tatu zimeamuliwa na moja bado inaendelea.
Dk Kolikoli alisema migogoro iliyowasilishwa hadi sasa imehusisha zaidi wawekezaji na wasuluhishi wa masoko ya mitaji, hususan madalali.
Alisema baadhi ya wawekezaji wamekuwa na malalamiko kuhusu maamuzi yaliyofanywa na madalali bila kuwashirikisha, huku wengine wakiwa na migogoro kuhusu fedha baada ya mauzo ya uwekezaji.
Alisema kujifunza kutoka kwa baraza lenye uzoefu zaidi kutaiwezesha baraza la masoko ya mitaji kujiandaa kwa ongezeko la kesi kadri ushiriki katika masoko ya mitaji unavyoendelea kukua.
Dk Kolikoli alisema baraza pia inaandaa mfumo wa usimamizi wa kesi utakaowawezesha wahusika kushiriki katika vikao kwa njia ya mtandao na kupata nakala za maamuzi bila kulazimika kufika katika baraza hilo.
MTAALAM katika Sekta ya Mafuta nchini Dkt Sajad Habib Rai amempongeza Makamu wa Rais Ndejembi kwa kuapishwa kwake kushika nafasi hiyo huku akisisitiza hana shaka na uwezo na uadilifu wake katika kulitumikia Taifa la Tanzania akimsaidia Rais Samia Suluhu Hassan
Akizungumza jijini Dar es Salaam siku moja baada ya uapisho wa Makamu Rais huyo Ikulu ya Cha Chamwino, Dodoma, Dkt Sajad amesema ana imani kubwa na Kiongozi huyo huku akimpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa uteuzi wa Ndejembi.
Dkt Sajad ambaye ni Meneja Mkazi wa Mansoor Industries nchini, amesema hana shaka na uwezo wa Ndejembi katika uongozi akisisitiza kwa sifa na uwezo alionao ni msaada tosha katika usaidizi kwa Dkt Samia Suluhu Hassan.
" Kwa kipindi kifupi alichohudumu katika Wizara ya Nishati kwa nafasi ya Uwaziri , Mheshimiwa Ndejembi amekuwa mtu muhimu aliyesimama kikamilifu katika kuahughulikia masuala mbalimbali, hii ni sifa ambayo siyo kila Kiongozi anayo" amesema Dkt Sajad
Amesema hatua ya Rais Samia Hassan kumteua na baadae jina lake kupitishwa na Bunge, kunatokana uwezo wake hatua iliyomfanya kiongozi huyo Mkuu wa nchi kujenga imani dhidi yake hivyo anapaswa kuendelea kumuonesha imani hiyo wakati huu anapomsaidia katika majukumu makubwa zaidi Kiongozi.
Mtaalamu huyo wa Nishati pamoja na Mawasiliano aliyeisaidia Serikali katika 'upigaji mafuta' bandarini kupitia ubunifu wake wa mfumo maalumu wa udhibiti wa mafuta (BIL) amewataka wananchi kumuamini Ndejembi sambamba na kumpa ushirikiano wakati huu anapotekeleza wajibu wake.
Pamoja na wananchi Dkt Sajad pia amewataka watendaji wote wa Serikali, Wabunge pamoja na wafanyabiashara nchini wakiwemo waliomo katika sekta ya mafuta kuendelea kumuunga mkono Makamu wa Rais Ndejembi ili aweze kutimiza kikamilifu majukumu yake ya kumsaidia Rais Samia na Taifa kwa ujumla.
Ndejembi ambaye amehudumu katika nafasi mbalimbali za utumishi pamoja na uongozi ikiwemo ya Waziri wa Utumishi baadae Waziri wa Nishati ameapishwa jana kushika nafasi hiyo ya Makamu wa Rais baada ya mtangulizi wake Dkt Emmanuel Nchimbi kujiuzuru hivi karibuni.
Natumai hujambo Mama yangu, na unaendelea vema na majukumu yako mazito ya kuliongoza na kulijenga Taifa letu la Tanzania. Najua dhamana uliyonayo si ndogo, na najua kila siku mbele yako inakuja na majukumu, matarajio na wakati mwingine changamoto zinazohitaji hekima, uvumilivu na moyo wa ziada.
Mama Rais Samia, waswahili wanasema, “barua ni nusu ya kuonana.” Nami nimeona nikutumie barua hii ya wazi, nikitumaini maudhui yake uyapokee kama vile unavyomuona mwanao anayeketi mbele yako na kukuambia yaliyo moyoni mwake. Siandiki kwa nia ya kukufundisha uongozi, kwa sababu najua dhamana uliyonayo na uzoefu unaokufanya uwe ulipo leo. Naandika kwa sababu mimi ni Mtanzania ninayependa kuona nchi yangu ikiendelea kusonga mbele.
Mama Rais Samia, nimetafakari sana yote yaliyotokea, yanayoendelea kutokea na hata yale tunayodhani yanaweza kutokea huko mbele. Nimetafakari kuhusu taifa letu, kuhusu uongozi wako, kuhusu changamoto zinazojitokeza na kuhusu matarajio makubwa waliyonayo Watanzania. Ghafla, nikajikuta nimekaa mezani, kalamu ikiwa mkononi, nikaanza kukuandikia barua hii ya wazi.
Mama Rais Samia, huenda barua hii isiwe na muhuri wa Serikali, isiwe na nembo ya taasisi yoyote na wala isiwe na cheo chochote nyuma ya jina langu. Lakini ina kitu kimoja muhimu: ina moyo wa Mtanzania anayekuandikia kiongozi wake kwa heshima, kwa nia njema na kwa matumaini kwamba ujumbe huu utakufikia.
Mama Rais Samia, najua kipindi hiki si rahisi. Najua katika safari ya uongozi kuna nyakati ambazo mambo huenda kama ulivyopanga, lakini pia kuna nyakati ambazo matukio huja ghafla na kulazimisha kiongozi kutafakari upya hatua zinazofuata. Ndiyo maana nimeona nikufikishie ujumbe huu mmoja muhimu: Usikate tamaa, Mama. Endelea kujenga nchi yetu.
Rais wangu Dkt. Samia, katika siasa na uongozi, kuondoka kwa mtu mmoja hakupaswi kuwa sababu ya safari ya taifa kusimama. Watu huja na kuondoka, nafasi hubadilika na nyakati hubadilika, lakini nchi hubaki. Tanzania bado ipo, Watanzania bado wana matumaini na mbele yako bado kuna kazi kubwa ya kulijenga taifa hili.
Rais wangu Dkt. Samia, si kila hatua ya uongozi huwa nyepesi. Kuna nyakati ambazo kiongozi hukutana na changamoto zisizotarajiwa, mabadiliko ya kisiasa na maamuzi ya watu aliokuwa akifanya nao kazi kwa karibu. Hayo ni sehemu ya safari ya uongozi, na katika nyakati kama hizi, kinachohitajika zaidi ni utulivu wa akili, hekima na uwezo wa kuangalia mbele.
Rais wangu Dkt. Samia, tunafahamu kwamba kipindi hiki si cha kawaida baada ya Makamu wako Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi, kutangaza kujiuzulu nafasi hiyo. Lakini tukio hilo lisikufanye uone kama safari ya Serikali yako imepata mwisho. Badala yake, lichukulie kama sehemu ya changamoto za uongozi na sababu ya kuongeza nguvu katika kusimamia majukumu uliyopewa na Watanzania.
Rais wangu Dkt. Samia, usife moyo. Usiruhusu changamoto za kisiasa zikupunguzie kasi ya kazi ya kulijenga taifa. Endelea kuwa mtulivu, sikiliza sauti mbalimbali, tafakari kwa kina na chukua maamuzi yenye maslahi mapana ya Tanzania. Wakati mwingine, uimara wa kiongozi hauonekani wakati mambo yako sawa; huonekana zaidi pale anapokutana na mawimbi.
Rais wangu Dkt. Samia, una dhamana kubwa mbele ya Watanzania. Ulipoomba ridhaa yao katika uchaguzi mkuu wa Oktoba, 2025, uliwaahidi mambo mbalimbali kuhusu mustakabali wa nchi yao. Sasa wananchi wanataka kuona ahadi hizo zikigeuka kuwa matokeo. Kazi iliyopo mbele yako si kuangalia sana nani ameondoka au nani amebaki, bali kuhakikisha Tanzania inaendelea kusonga mbele.
Rais wangu Dkt. Samia, ongeza juhudi katika uchumi, ajira, elimu, afya, kilimo, miundombinu na uwekezaji. Lakini zaidi ya yote, endelea kuangalia maisha ya Mtanzania wa kawaida anayehangaika kutafuta chakula, mzazi anayesubiri huduma bora za afya kwa familia yake, kijana anayehitaji ajira na mfanyabiashara anayehitaji mazingira rafiki ya kufanya biashara.
Rais wangu Dkt. Samia, endelea kusikiliza wananchi. Nguvu kubwa ya Serikali haipo katika ofisi kubwa wala magari ya misafara; ipo katika uwezo wa kusikia kilio cha wananchi na kukifanya kuwa sehemu ya ajenda ya Serikali kama ufanyavyo wewe. Wananchi wanahitaji kuona kwamba uongozi wao unawasikia, unawajali na unafanya kazi kwa ajili yao.
Rais wangu Dkt. Samia, Tanzania ni kubwa kuliko mtu mmoja, nafasi moja au tukio moja la kisiasa. Serikali ina taasisi, ina mifumo na ina watendaji. Kwa hiyo, mabadiliko katika nafasi moja yasiruhusiwe kuvuruga mwelekeo wa taifa. Kazi ya Serikali lazima iendelee, miradi iendelee, uchumi uendelee na huduma kwa wananchi ziendelee kuboreshwa.
Rais wangu Dkt. Samia, uongozi hupimwa zaidi wakati wa changamoto kuliko wakati mambo yanapokuwa rahisi. Hiki kinaweza kuwa kipindi kigumu, lakini pia kinaweza kuwa nafasi muhimu kwako kuonyesha zaidi uwezo wako wa kiuongozi, uvumilivu, hekima na weledi katika kuliongoza taifa letu.
Rais wangu Dkt. Samia, Watanzania wanahitaji amani, utulivu na mazingira yatakayowawezesha kufanya kazi na kujenga maisha yao. Wanahitaji kuona tofauti za kisiasa hazigeuki kuwa kikwazo cha maendeleo. Wanahitaji kuona taasisi za Serikali zikifanya kazi kwa ufanisi na viongozi wakitumia madaraka yao kwa ajili ya maslahi ya wananchi.
Rais wangu Dkt. Samia, usikubali changamoto ya leo ikufanye usahau wajibu wa kesho. Historia ya uongozi haijengwi kwa namna kiongozi anavyokabiliana na siku nzuri pekee, bali pia kwa namna anavyosimama imara wakati wa misukosuko na kuhakikisha taifa halianguki.
Rais wangu Dkt. Samia, endelea na kazi. Jenga Tanzania. Timiza yale uliyowaahidi Watanzania. Ongeza maarifa, hekima, juhudi na weledi. Wakati huu unahitaji uongozi unaotazama mbele, unaotanguliza taifa na unaojua kwamba dhamana uliyonayo ni kubwa kuliko changamoto yoyote ya kisiasa inayoweza kujitokeza.
Rais wangu Dkt. Samia, changamoto zitapita, watu watabadilika na nyakati zitabadilika, lakini Tanzania itaendelea kubaki. Kinachohitajika sasa ni uongozi wenye utulivu, hekima, uadilifu, uwajibikaji na maono ya mbali.
Rais wangu Dkt. Samia, huu ndiyo wakati wa kuangalia mbele zaidi kuliko nyuma. Huu ndiyo wakati wa kuimarisha timu yako, kusimamia kwa karibu utekelezaji wa mipango ya Serikali na kuhakikisha kila ahadi iliyotolewa kwa wananchi inapata majibu katika vitendo.
Rais wangu Dkt. Samia, ujumbe wangu kwako ni mmoja tu: Usikate tamaa. Jenga nchi. Endelea kufanya kazi kwa ajili ya Watanzania. Tanzania inahitaji uongozi unaotazama mbele.
Ni mimi mwanao Rashid Mtagaluka
Mbagala, Dar es Salaam
28/08/2026
Simu: 0718 406 242
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amewasili leo, tarehe 30 Agosti 2026, jijini Belgrade, Jamhuri ya Serbia, kumwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Mkutano Maalum wa Ngazi ya Juu wa Kumbukumbu ya Miaka 65 tangu kufanyika kwa Mkutano wa Kwanza wa Wakuu wa Nchi wa Harakati za Nchi Zisizofungamana na Upande Wowote (NAM).
Rais Dkt. Mwinyi amewasili akiwa ameambatana na ujumbe wake, akiwemo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo, pamoja na viongozi wengine wa Serikali.
Katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Nikola Tesla, Rais Dkt. Mwinyi amepokelewa na Naibu Waziri Mkuu ambaye pia ni Waziri wa Uchumi wa Jamhuri ya Serbia, Mhe. Adrijana Mesarović, pamoja na Balozi wa Tanzania nchini Italia ambaye pia anaiwakilisha Tanzania katika Jamhuri ya Serbia, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk.
.jpeg)
Dkt. Mwigulu ameyasema hayo leo Jumapili, Agosti 30, 2026, katika maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 25 ya Jimbo Katoliki la Mpanda, yaliyofanyika mkoani Katavi, ambapo amesema Serikali inatambua mchango wa Kanisa Katoliki katika maendeleo ya nchi, hususan katika sekta za elimu, afya na huduma za kiroho.
“Serikali inatambua mchango wa Kanisa na baba Askofu. Kila tunapotaja maendeleo ya nchi yetu, kuanzia mwanzo mpaka hapa tulipofika, hatuwezi kuyataja kwa kina maendeleo hayo bila kutaja mchango wa Kanisa.”
Amesema ushirikiano kati ya Serikali na Kanisa umeendelea kuwa muhimu katika kuhakikisha huduma za kijamii na shughuli za maendeleo zinaimarika, akisisitiza kuwa milango ya Serikali itaendelea kuwa wazi kwa Kanisa na taasisi nyingine za dini katika masuala yanayolenga ustawi wa wananchi.
“Niwahakikishie Serikali itaendelea kushirikiana na Kanisa na popote pale mlipo na jambo msisite, milango yetu iko wazi ili tuweze kuhakikisha kwamba tufanye jambo lolote linalotufurahisha.”
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ametoa maelekezo kwa viongozi wa Mkoa wa Katavi na mamlaka husika kuharakisha utekelezaji wa miradi ya barabara, maji na umeme, akisisitiza kuwa wananchi wanapaswa kupata huduma hizo kwa wakati.
Amesema maandalizi ya kukabiliana na uwezekano wa kutokea kwa El Niño yanapaswa kwenda sambamba na hatua za vitendo, ikiwemo ujenzi na uboreshaji wa mifereji na madaraja ili kupunguza athari za mafuriko.
Kuhusu huduma za maji, Waziri Mkuu ameitaka Wizara ya Maji na wahusika wa mradi wa maji Mpanda kuhakikisha wananchi wanapata huduma hiyo ifikapo Desemba 2026, huku akisisitiza pia kuharakishwa kwa miradi ya barabara inayounganisha Katavi na mikoa jirani.
Aidha, Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea kuchukua hatua za kuboresha mazingira ya haki kwa wananchi, akitangaza kuwa Serikali inaelekea kufuta sheria inayohusu utaifishaji wa mifugo, akieleza kuwa hatua hiyo inalenga kuondoa changamoto za wananchi kunyang’anywa mifugo yao.
“Katika Bunge hili linaloendelea tunakwenda kufuta sheria ya utaifishaji wa mifugo... kumekuwepo na majeraha makubwa ya watu kunyang’anywa katika baadhi ya maeneo. Tunataka tuondoe hayo ili kuhakikisha kwamba wananchi wetu wanaepukana na hayo.”
Pia ametoa maelekezo kwa wasimamizi wa sheria kuacha kukamata vitendea kazi vya wananchi kama pikipiki, bajaji na magari katika utekelezaji wa sheria za makosa mbalimbali, akisisitiza umuhimu wa kutumia utaratibu wa kisheria wa adhabu na faini.
Kwa upande wake, Askofu wa Jimbo Katoliki la Mpanda, Mhashamu Baba Askofu Eusebius Nzigilwa, amemshukuru Waziri Mkuu kwa kutenga muda na kushiriki katika maadhimisho hayo, akisema uwepo wake umeonesha heshima na kuthaminiwa kwa Jimbo la Mpanda na Kanisa Katoliki Tanzania.
“Ninakushukuru sana. Tunaona hiyo ni heshima kwa Jimbo letu na kwa Kanisa Katoliki Tanzania, na hivyo tunaomba Mwenyezi Mungu azidi kuwaongoza na kuwajalia neema na hekima katika kutuongoza sisi raia na wananchi wenu.”
Naye Balozi wa Baba Mtakatifu nchini Tanzania anayemaliza muda wake, Mhashamu Askofu Mkuu Angelo Accattino, amesisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano kati ya Serikali na Kanisa Katoliki, akisema ushiriki wa viongozi wa Serikali na viongozi wa dini mbalimbali katika maadhimisho hayo ni ishara ya mahusiano mema kwa ajili ya ustawi wa jamii.
Maadhimisho hayo yamefanyika katika kuadhimisha miaka 25 tangu kuanzishwa kwa Jimbo Katoliki la Mpanda mwaka 2001, huku viongozi wa Kanisa wakieleza kuwa katika kipindi hicho Jimbo limepiga hatua katika huduma za kichungaji, elimu, afya na ujenzi wa miundombinu kwa ajili ya jamii.
Waziri Mkuu amewapongeza viongozi wa Kanisa, waamini na wananchi wa Jimbo Katoliki la Mpanda kwa kufanikisha Jubilee hiyo, akiwataka kuendelea kushirikiana na Serikali katika kujenga jamii yenye amani, mshikamano na maendeleo.

.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)







.jpeg)







.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)





















.jpeg)



.jpeg)