Benki ya NMB imewahakikishia wafanyabiashara kuendelea kuwapatia masuluhisho ya kifedha yanayolenga mahitaji ya sekta mbalimbali za uchumi. Kauli hiyo ilitolewa mwishoni mwa wiki katika Jukwaa la NMB Business Executive Network 2026 lililowakutanisha zaidi ya wafanyabiashara 300 kutoka Dar es Salaam na Pwani.

Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB, Filbert Mponzi, alisema benki hiyo imeanzisha Madawati ya Kisekta ili kutoa huduma zinazolingana na mahitaji ya sekta kama madini, ujenzi, utalii, kilimo, afya na elimu. Alisema masuluhisho hayo yanajumuisha Asset Financing, Bid Bond, Advance Payment Guarantee na Performance Guarantee.

Katika jukwaa hilo, NMB pia ilitambulisha tuzo mbili za kimataifa ilizotunukiwa mwaka huu ambazo ni Tuzo ya Benki Bora zaidi kwa Wafanyabiashara Tanzania 2026 kutoka jarida la Euromoney na Tuzo ya Benki Bora zaidi kwa Wafanyabiashara Tanzania 2026 kutoka jarida la Global Finance, zikidhihirisha kutambuliwa kwake kimataifa kwa ubora wa huduma.

Jukwaa hilo lilitoa nafasi kwa wafanyabiashara na viongozi wa NMB kujadiliana kuhusu mahitaji ya sekta binafsi na namna ya kuendelea kuimarisha ushirikiano unaochochea ukuaji wa biashara na uchumi wa Tanzania.
Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa Benki ya NMB, Filbert Mponzi (kulia), Mkuu wa Idara ya Biashara NMB, Deogratias Shirima (kushoto) wakifurahia tuzo za Benki Bora ya Huduma kwa Wafanyabiashara Wadogo na wa Kati (SMEs), zilizotolewa na Euromoney na Global Finance wakati wa hafla iliyowakutanisha NMB na Mtandao wa Wafanyabiashara Wakubwa Wanaohudumiwa na benki hiyo ‘NMB Business Executive Network’ iliyofanyika Ijumaa jijini Dar es Salaam. Wapili kushoto ni Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya TTI, Leonard Shayo na wa pili kulia ni Mkurugenzi wa Kampuni ya High Quality, Selina Letara.









Na Mwandishi Wetu

WADAU wa mchezo wa uogeleaji Tanzania wanatarajiwa kunufaika na mafunzo ya kiwango cha kimataifa kupitia programu ya wiki tatu iliyolenga kukuza vipaji vya waogeleaji vijana, kuimarisha uwezo wa makocha wa wazawa, pamoja na kuwaelimisha wazazi kuhusu namna bora ya kuwaunga mkono wanamichezo katika safari yao ya mafanikio.

Programu hiyo iliyopewa jina la Tanzania Performance Development Series 2026, imeandaliwa na RaceBetter kwa ushirikiano na Monti AquaForce, na itafanyika kuanzia Julai 28 hadi Agosti 14 katika Kampasi ya Mikocheni ya Shule ya Kimataifa ya Monti, jijini Dar es Salaam.

Mafunzo hayo yataongozwa na kocha mashuhuri wa kimataifa wa uogeleaji na mwanzilishi wa RaceBetter, Ben Lee, ambaye anatarajiwa kuwasili jijini Dar es Salaam Jumatatu kutokea nchini Marekani.

Mwanzilishi na Mkurugenzi wa Shule ya Kimataifa ya Monti, Fatma Fernandes, alisema mpango huo unaashiria mwanzo wa ushirikiano wa muda mrefu unaolenga kuimarisha maendeleo ya mchezo wa uogeleaji nchini Tanzania kwa kuunganisha utaalamu wa kimataifa na uongozi wa ndani ili kujenga mfumo endelevu wa kukuza vipaji kuanzia ngazi ya msingi hadi ushindani wa kiwango cha juu.

Mfululizo wa mafunzo hayo utaanza kwa Warsha ya Maendeleo ya Makocha itakayofanyika Julai 28 hadi 30, ikiwakutanisha makocha wa uogeleaji, walimu na viongozi wa vilabu vya uogeleaji. Warsha hiyo inalenga kuboresha viwango vya ufundishaji huku ikiwapa makocha wa ndani fursa ya kujifunza na kufanya kazi bega kwa bega na Ben Lee katika kipindi chote cha kambi za mafunzo kwa wanamichezo.

Fatma alisema pia kutakuwa na kambi tatu za mafunzo kulingana na makundi ya umri wa washiri.

“Kambi kwa waogeleaji wenye umri wa miaka 6 hadi 8, itafanyika kuanzia Julai 30 hadi Agosti 1. Itafuatiwa na Kambi kwa waogeleaji wenye umri wa miaka 9 hadi 12 kuanzia Agosti 3 hadi 7. Programu hiyo itahitimishwa na Kambi kwa waogeleaji wenye umri wa miaka 13 na kuendelea, itakayofanyika kuanzia Agosti 10 hadi 14.

“Aidha, kutakuwa na mfululizo wa mafunzo kwa wazazi, yatakayotolewa bila malipo sambamba na kambi hizo. Vipindi hivyo vitajikita katika lishe na urejeshaji wa nguvu kwa wanamichezo, kujenga kujiamini na ustahimilivu, pamoja na kuwasaidia wazazi kujenga utaratibu mzuri wa maisha unaowawezesha watoto wao kufanikiwa ndani na nje ya bwawa la kuogelea,” alisema.

Alisema programu hiyo itafanyika katika bwawa la kuogelea la mita 25 la Shule ya Kimataifa ya Monti, lenye viwango vya kimataifa kwa mashindano ya kozi fupi, na hivyo kuwapatia washiriki mazingira bora ya mafunzo.

Aliongeza kuwa idadi ya washiriki imewekewa ukomo ili kuhakikisha kila mshiriki anapata mafunzo ya karibu katika vikundi vidogo na ushauri wa moja kwa moja kutoka kwa wakufunzi.

Akizungumza kuhusu programu hiyo, Ben Lee, ambaye ana uzoefu mkubwa wa kufundisha waogeleaji kuanzia ngazi ya maendeleo, vyuo vikuu hadi Olimpiki, alisema lengo kuu si kuwajengea waogeleaji kasi pekee, bali kuwajenga kama watu.

“Lengo letu si kuzalisha waogeleaji wenye kasi zaidi pekee. Tunataka kuwasaidia watu kuwa na uwezo zaidi, kujiamini zaidi na kuwa tayari kwa fursa na changamoto zitakazokuja mbele yao,” alisema.

Katika kipindi chake cha ukocha, Ben Lee amewafundisha wanamichezo wengi waliofanikiwa kujiunga na programu maarufu za NCAA nchini Marekani na kushiriki mashindano ya kimataifa. Pia amefanya kazi na vilabu vya uogeleaji, shule na mashirikisho ya kitaifa katika nchi mbalimbali duniani.


Na Victor Masangu, Kibaha

Mwenyekiti wa  Jumuiya ya wazazi Taifa Ndg. Fadhili Maganya amewaasa viongozi wa chama cha mapinduzi  (CCM)  ngazi  za Wilaya pamoja na   Mkoa wa Pwani  kuhakikisha kwamba  wanalivalia njuga  suala la kero  ya  migogogoro ya ardhi sambamba na kusikiliza   changamoto mbali mbali   zinazowakabili wananchi na kuzitafutia ufumbuzi.

Kauli hiyo ameitoa wakati wa ziara yake ya  kikazi yenye lengo la   kukijenga chama pamoja na kukagua uhai wake na kuimarisha jumuiya zake sambamba na kuangalia mwenendo mzima wa utekelezaji wa ilani  ikiwemo kukagua na kutembelea  baadhi ya miradi mbali mbali  ya maendeleo.

Mwenyekiti huyo  amebainisha kuwa katika ziara hiyo pia imelenga kukutana na viongozi mbali mbali wa serikali na kupokea taarifa zao  zinazohusiana  na suala zima la  utekelezaji wa kazi  zao  ambazo wanazifanya katika   maeneo yao  kwenye  nyanja mbali mbali za kimaendeleo.

"Nimeanza ziara yangu ya kikazi katika Wilaya ya Kibaha na lengo kubwa na kwamba ziara hii ni ya kikazi na lengo lake kubwa ni kuangalia uhai wa chama jinsi ilivyo, pamoja na jumuiya zake ikiwa sambamba na kuweza kuangalia na kutembelea miradi mbali mbali ya kimaendeleo na kuzungumza na wanachama," amebainisha Mwenyekiti huyo.

Pia Mwenyekiti huyo   amewasihi  wanachama  na viongozi kuhakikisha kwamba wanaachana  kabisa na tabia ya  kuwasikiliza baadhi ya  wanaharakati ambao  wamekuwa wakibeza mambo mbali mbali ambayo  yanatekelzwa  na serikali ya awamu ya sita  na badala yake  wajikite zaidi katika kumuunga mkono Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi ambazo anazifanya.

Pia amewahimiza madiwani na   viongozi wengine kuhakikisha wanaweka misingi imara ya  kusimamia  utoaji wa fursa za  mikopo ya asilimia 10  ambayo  inatolewa na halmashauri kwa lengo la kuwasaidia wajasiriamali waweze kujikwamua kiuchumi na kuondokana na umasikini .

Aidha Mwenyekiti huyo hakusita kumpongeza kwa dhati Mkuu wa Mkoa wa Pwani kwa  kuweza kuchapa kazi  kwa bidii pamoja na kuendelea kutekeleza ilani kwa vitendo katika suala zima la kusimamia fedha ambazo zimekwenda kutekeleza miradi mbali mbali  ya maendeleo pamoja na mkurugenzi mtendaji wa Halmashauru ya Manispaa ya Kibaha Dkt. Rogers Shemwelekwa.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Pwani Alhaj Abubakari Kunenge akitoa salama zake amesema kwamba Mkoa wa Pwani imeweza kuendelea kutekeleza miradi mbali  mbali ya maendeleo ikiwemo sekta ya elimu, afya, umeme, miundombinu ya barabara pamoja na ujenzi wa viwanda.

Naye Mjumbe wa halmashauri kuu ya   chama cha mapinduzi (CCM) Taifa   Hamoud Jumaa amesema kwamba lengo lake kubwa ni kuendelea kushirikiana bega kwa bega katika kuhakikisha  chama cha serikali kinaendelea kuwa na mahusiano mazuri ikiwemo sambamba na kutekeleza ilani ya chama.  

Mwenyekiti wa Jumuiya ya wazazi Mkoa wa Pwani Jackson Kituka amebainisha kuwa ni jukumu la wanachama kuendelea  na kuweza kushikamana katika kukijenga chama  ikiwa sambamba na kuiimarisha  zaidi kwa vitendo jumuiya zake zote.

 Mwenyekiti wa chama cha mapinduzi(CCM) Wilaya ya Kibaha mjini Mwalimu Mwajuma Nyamka  amempongeza kwa dhati Mwenyekiti huyo  kwa kuamua kufanya ziara ambayo itaweza kuleta uhai wa chama pamoja na kuimarisha jumuiya zake ikiwa pamoja na kutembelea miradi mbali mbali ya maendeleo.

Mbunge wa Jimbo la Kibaha mjini Silvestry Koka  amempongeza Mwenyekiti wa jumuiya  ya wazazi Taifa kwa kutekeleza ilani ya chama kwa vitendo ikiwa sambamba na kuweza kuona umuhimu wa kufanya ziara yake ya kikazi ambayo itaweza kuleta  matokeo chanya katika suala zima la kukiimarisha chama pamoja na jumuiya zake kwa pamoja.

 Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Taifa ameanza ziara yake rasmi ya kikazi katika Mkoa wa Pwani ambapo ameanza  katika Wilaya ya Kibaha ambapo ameweza kutembelea baadhi ya miradi ya maendeleo katika Zahanati ya Kilimahewa iliyopo kata ya Tangini, Kituo cha afya mlandizi pamoja na  kutembelea mradi wa ujenzi wa stendi ya mabasi Mlandizi.





                                

 


Mkuu wa wilaya ya Bahi Mhe. Joachim Thobias Nyingo amekabidhi gari jipya aina ya ‘Toyota Pickup’ kwa Meneja wa Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) wa wilaya hiyo Mha. Hopeness Liundi huku akitoa wito wa kutumia vizuri kitendea kazi hicho kwa kuongeza kasi ya utendaji kazi kwa tija ili kufikia lengo la kumtua mama ndoo kichwani kwa kuwafikishia huduma ya Majisafi ya bomba wananchi wa wilaya hiyo.

Hafla ya makabidhiano hayo imefanyika katika ofisi ya Meneja RUWASA Mkoa wa Dodoma Julai 27, 2026 na kuhudhuriwa na Meneja wa Mkoa huo Mha. Beatrice Kasimbazi pamoja na watumishi wengine wa mkoa huo.

Akizungumza kabla ya kuzindua na kukabidhi gari hilo, Mhe. Nyingo aliishukuru Serikali ya awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuiwezesha RUWASA na kuboresha utendaji wao wa kazi ikionesha dhamira ya dhati ya serikali kuwafikishia wananchi huduma muhimu ya majisafi ya bomba.

Hivi karibuni, Serikali kupitia RUWASA ilinunua na kugawa magari 22 katika mikoa na wilaya mbalimbali nchini ikiwa ni hatua ya kuboresha na kuimarisha utendaji wa taasisi katika kusimamia na kufuatilia miradi na huduma ya maji katika maeneo ya vijijini.

Katika hatua nyingine, Mhe. Mkuu wa wilaya Nyingo amemkaribisha Meneja mpya wa RUWASA wa mkoa wa Dodoma Beatrice Kasimbazi ambaye amehamishiwa mkoani humo akitokea mkoa wa Pwani, huku akitoa wito kwa watumishi wa wilaya hiyo kumpokea na kumpa ushirikiano katika kutekeleza majukumu mbalimbali ya serikali na kuwahudumia wananchi.








Na Mwandishi wetu

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewaapisha Naibu Makatibu Wakuu wawili na kushuhudia viongozi wanne wakila Kiapo cha Uadilifu kwa Viongozi wa Umma, huku akiwataka kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu, ushirikiano, uwajibikaji na kuzingatia maslahi ya wananchi.

Akizungumza katika hafla iliyofanyika Ikulu, Tunguu, Zanzibar, Rais Samia amesema uteuzi wa viongozi hao unaonesha imani ambayo Serikali imewawekea, hivyo wanapaswa kuhakikisha wanatoa huduma bora, kufanya kazi kwa weledi na kuleta matokeo yanayogusa maisha ya Watanzania.

Rais Samia ameielekeza Ofisi ya Makamu wa Rais kuendelea kuimarisha usimamizi wa masuala ya Muungano kwa kushughulikia changamoto zinazojitokeza kupitia ushirikiano, ili kuendelea kuulinda na kuuimarisha Muungano wa Tanzania. Pia amesisitiza umuhimu wa kusimamia kwa karibu programu za uhifadhi wa mazingira na hatua za kukabiliana na changamoto zinazotishia ustawi wa Taifa.

Aidha, ameagiza Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kuendelea kuboresha usimamizi wa watumishi wa umma kwa kuweka mazingira yatakayowawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na kuongeza ubora wa utoaji wa huduma kwa wananchi.

Katika sekta ya uchukuzi, Rais Samia amesisitiza kuongezwa kasi ya utekelezaji wa miradi ya reli, barabara, bandari na meli, pamoja na kutathmini fursa za kupanua biashara ya anga ya Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) ili kuongeza mchango wake katika maendeleo ya uchumi.

Kwa upande wa sekta ya sheria, ameitaka Wizara ya Katiba na Sheria kuendelea kuimarisha upatikanaji wa haki kwa wananchi kupitia kampeni za msaada wa kisheria, ili huduma hizo ziweze kuwafikia wananchi wengi zaidi kwa wakati.

Vilevile, Rais Samia ameitaka Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE) kuongeza juhudi katika kukuza biashara na kuboresha usimamizi wa maonesho ya biashara nchini. Pia ameliagiza Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) kuimarisha ulinzi na usimamizi wa hifadhi za taifa na rasilimali za utalii, akieleza kuwa sekta hiyo ni nguzo muhimu ya uchumi wa Taifa.

Kwa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), Rais Samia amesisitiza umuhimu wa kuendelea kuimarisha nafasi yake kama chombo cha Serikali na sauti ya Taifa kwa kuongeza ubora wa maudhui, weledi wa watumishi na ufanisi katika utoaji wa huduma za habari.

Walioapishwa ni Dkt. Latifa Mohammed Khamis, aliyeteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais anayeshughulikia masuala ya Muungano, pamoja na Bi. Prisca Burton Lwangili, aliyeteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

Viongozi wengine walioapa Kiapo cha Uadilifu ni Bw. Ephraim Balozi Mafuru, Mkurugenzi Mkuu wa TANTRADE; Bw. Salum Nassor Mnuna, Mkurugenzi Mkuu wa EWURA; Bw. Massana Gibril Mwishawa, Kamishna wa Uhifadhi wa TANAPA; na Bi. Asha Dachi Mbaruk, Mkurugenzi Mkuu wa TBC.



Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) leo, Julai 27, imewasha vifaa vya usikivu (Cochlear Implant) kwa watoto saba waliopandikizwa vifaa hivyo, ikiwa ni mwendelezo wa huduma za kibobezi za upandikizaji huo zilizozinduliwa rasmi mwaka 2017 ambapo hadi sasa hospitali imefanikiwa kuwafanyia upasuaji wa kupandikiza vifaa vya usikivu wagonjwa 115 na kuwa hospitali ya kwanza barani Afrika.

Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Bw. Emmanuel Tayari, amepongeza hatua hiyo na kubainisha kuwa serikali inaendelea kuweka mikakati thabiti ya kusogeza huduma za kibobezi karibu na jamii ili kuliokoa Taifa dhidi ya changamoto za kiafya zinazoweza kuepukika.

Aidha, Mkurugenzi Mtendaji wa MNH Dkt. Dellilah Kimambo, ameeleza kuwa tangu mwaka 2017 Wizara ya Afya kupitia Muhimbili iliazimia kimkakati kuleta huduma za kibobezi nchini lengo ikiwa ni kuzuia wagonjwa kusafiri nje ya nchi na kupunguza gharama kubwa walizokuwa wakizibeba wananchi na kupunguza rufaa za matibabu nje ya nchi ambayo yalikua yanagharimu takribani shillingi mil 120 kwa mgonjwa mmoja ambapo kwa sasa hivi matibabu hayo yanatolewa hapa hapa Nchini kwa gaharama ya TZS. 45 Mil.

"Sasa hivi duniani inajulikana kwamba mtoto mwenye matatizo ya kusikia akipandikizwa kifaa hiki kwa wakati husika, ataweza kusikia kama kawaida na kuepuka changamoto za kuwa kiziwi tulipoamua kuleta huduma hii hapa nchini, wagonjwa wengi waliokuwa wakikosa huduma hapo awali sasa wamefaidika, na inawawezesha kuendelea na maisha yao ya kawaida,"  amesema Dkt. Kimambo.

Muhimbili inaendelea kuboresha huduma hii ambayo inatajwa kuwa unatajwa kuwa muhimu katika kuhakikisha watoto wanaozaliwa au kupata changamoto za usikivu wanapata fursa sawa ya kusoma na kushiriki katika ujenzi wa Taifa bila kikwazo cha ulemavu wa kutosikia.












 

 Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Serikali imepanga kuwaweka kambini wanafunzi 1,050 waliofanya vizuri zaidi katika Mtihani wa Kidato cha Sita mwaka 2026 na kuchaguliwa kunufaika na mpango wa Samia Scholarship, ambapo watapatiwa mafunzo maalumu ya kuwaandaa kabla ya kuanza masomo yao ya elimu ya juu.

Kambi hiyo itafanyika katika Chuo Kikuu cha Nelson Mandela African Institution of Science and Technology (NM-AIST) jijini Arusha, ambako wanafunzi hao watapata mafunzo mbalimbali yatakayowajengea uwezo wa kitaaluma, uongozi na ubunifu.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma leo, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, amesema mpango huo unatekelezwa kwa maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ukiwa na lengo la kuibua, kukuza na kuendeleza vipaji vya wanafunzi waliofanya vizuri katika masomo ya Sayansi, Teknolojia, Uhandisi na Hisabati (STEM) ili kuzalisha wataalamu watakaochochea maendeleo ya taifa na uchumi wa kisasa.

Profesa Mkenda amesema kati ya wanafunzi hao, 1,000 watapatiwa ufadhili wa kusoma katika vyuo vikuu vya ndani ya nchi, huku wanafunzi 50 bora zaidi wakipewa fursa ya kuendelea na masomo katika vyuo vikuu vya nje ya nchi kwenye fani zinazohitajika katika uchumi wa kidijitali.

Ameeleza kuwa wanafunzi hao wametokana na tahasusi za PCM (Physics, Chemistry and Mathematics), PCB (Physics, Chemistry and Biology), CBG (Chemistry, Biology and Geography), PMG (Physics, Mathematics and Geography), CBA (Chemistry, Biology and Agriculture) pamoja na PMC (Physics, Mathematics and Computer Science).

Kwa mujibu wa Waziri huyo, wanufaika wa ufadhili wa ndani wanapaswa kuomba udahili katika vyuo vikuu vya Tanzania kusomea shahada za Hisabati, Sayansi, Uhandisi au Tiba. Baada ya kupata udahili, watajaza fomu za kujiunga rasmi na mpango wa Samia Scholarship, ambapo Serikali itagharamia asilimia 100 ya ada na gharama za masomo yao.

Aidha, amesema majina ya wanafunzi wote waliochaguliwa yamechapishwa kwenye tovuti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, na kuwataka wahitimu wa Kidato cha Sita kuyakagua pamoja na kufuata taratibu zote zilizowekwa ili kukamilisha mchakato wa kupata ufadhili huo.

Akizungumzia wanafunzi 50 watakaopelekwa kusoma nje ya nchi, Profesa Mkenda amesema wameteuliwa kutoka katika tahasusi za PCM, PMG na PMC, ambazo zinahitaji uwezo mkubwa wa Hisabati ya Juu (Advanced Mathematics).

Amefafanua kuwa uteuzi huo umezingatia alama halisi za mtihani (raw scores) badala ya daraja la ufaulu pekee, akibainisha kuwa wanafunzi wengi wanaweza kupata daraja la "A", lakini wakatofautiana kwa idadi ya alama walizopata.

Profesa Mkenda amesisitiza kuwa Serikali imezingatia uwazi na uadilifu katika mchakato mzima wa uteuzi ili kulinda hadhi ya mpango wa Samia Scholarship. 

Amesema mwanafunzi yeyote mwenye mashaka kuhusu kutokuwamo kwenye orodha anaweza kuwasiliana na Wizara ya Elimu kwa ajili ya kupata ufafanuzi wa alama zake kupitia Baraza la Mitihani la Tanzania (NECTA).

Kwa upande mwingine, Waziri huyo amebainisha kuwa asilimia 58 ya wanafunzi waliochaguliwa wanatoka katika shule za serikali, huku asilimia 42 wakitoka katika shule zisizo za serikali, akisisitiza kuwa uteuzi umefanyika kwa kuzingatia vigezo vya ufaulu bila kujali aina ya shule aliyosoma mwanafunzi.







Na Mwendishi Wetu,Korea
MWENYEKITI  wa Kundi la Afrika katika Kikao cha 48 cha Kamati ya Urithi wa Dunia, Balozi Pierre Faye, ameipongeza Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuandaa kikao cha pembeni kilicholenga kujadili mustakabali wa uhifadhi wa Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro na maeneo mengine ya Urithi wa Dunia.

Akizungumza katika kikao hicho kilichofanyika Julai 27, 2026, Busan, Balozi Faye alisema mkutano huo unaendana na malengo ya Mkataba wa Urithi wa Dunia unaohimiza nchi wanachama kuimarisha uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa maeneo ya urithi pamoja na kuendeleza juhudi za kuyahifadhi kupitia elimu na utoaji wa taarifa.

Alisema mikutano ya aina hiyo ina nafasi muhimu ya kuwakutanisha wadau kutoka sekta mbalimbali ili kujenga ushirikiano katika kulinda maeneo ya urithi wa asili kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Balozi Faye alieleza kuwa ingawa jukumu la msingi la kuhifadhi maeneo ya Urithi wa Dunia liko mikononi mwa nchi husika, jumuiya ya kimataifa pia ina wajibu wa kushirikiana kuhakikisha maeneo hayo yanaendelea kulindwa na kuhifadhiwa.

Aliisifu Tanzania kwa kutenga takribani asilimia 38 ya eneo lake kwa shughuli za uhifadhi, hatua iliyoifanya kuwa miongoni mwa nchi zinazoongoza duniani katika kulinda rasilimali za asili.

Alitaja maeneo ya Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro, Hifadhi ya Taifa ya Serengeti na Hifadhi ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro kuwa miongoni mwa maeneo ya Urithi wa Dunia yanayoifanya Tanzania kutambulika kimataifa katika sekta ya uhifadhi.

Akizungumzia Ngorongoro, Balozi Faye alisema eneo hilo linakabiliwa na changamoto zinazotokana na ongezeko la idadi ya watu, haki za wafugaji na matumizi ya ardhi, hali inayoongeza ushindani wa matumizi ya malisho na vyanzo vya maji.

Alibainisha kuwa changamoto hizo zimeweka shinikizo katika mfumo wa mwaka 1959 uliolenga kuweka uwiano kati ya shughuli za ufugaji wa jamii ya Wamaasai na uhifadhi wa mazingira.

Aidha, alisema Mkataba wa Urithi wa Dunia unatambua umuhimu wa kuwepo kwa uwiano kati ya maendeleo ya binadamu na uhifadhi wa mazingira, akisisitiza kuwa ushirikiano wa wadau mbalimbali ndio njia bora ya kuhakikisha Ngorongoro inaendelea kuhifadhi hadhi yake ya urithi wa kipekee duniani.

Balozi Faye alihitimisha kwa kupongeza mwitikio mkubwa wa washiriki wa kikao hicho na kutoa wito kwa wadau wote kuendelea kushirikiana na Tanzania kwa njia ya kujenga ili kupata suluhisho litakalowanufaisha wananchi, uhifadhi na jumuiya ya kimataifa kwa ujumla.


Na Mwandishi Wetu
SERIKALI  kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) na Shirika la Reli Tanzania (TRC) inaendelea kutekeleza mpango wa kujenga bandari kavu katika maeneo mbalimbali nchini ili kupunguza msongamano mkubwa wa malori jijini Dar es Salaam.

Kauli hiyo ilitolewa na Kaimu Mkurugenzi Msaidizi wa Huduma za Barabara kutoka Wizara ya Uchukuzi, Andrew Magombana, aliyemwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Profesa Godius Kahyarara, wakati wa kufungua Mkutano Mkuu wa Kwanza wa mwaka wa Chama cha Wasafirishaji wa Shehena kwa Barabara Tanzania (TRFA) uliofanyika jijini Dar es Salaam.

Magombana alisema kuwa miradi ya ujenzi wa bandari kavu mkoani Morogoro pamoja na vituo vya usafirishaji vya Malindi na Bahi inaendelea vizuri. Alieleza kuwa miradi hiyo ikikamilika itawezesha mizigo kuchukuliwa kutoka Morogoro na Dodoma badala ya Dar es Salaam, hatua itakayopunguza msongamano wa magari na kuharakisha usafirishaji wa mizigo kwa wateja.

Aliongeza kuwa Bandari Kavu ya Kwala, ambayo tayari imekamilika, imechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza msongamano wa malori jijini Dar es Salaam kwa kuboresha ufanisi wa ushughulikiaji na usafirishaji wa mizigo. Pia aliipongeza TRFA kwa kushiriki kikamilifu katika utoaji wa huduma za usafirishaji kupitia bandari hiyo, akisema imeongeza ufanisi katika sekta ya lojistiki.

Magombana pia aliisifu TRFA kwa ushirikiano wake na Serikali kupitia majukwaa mbalimbali ya sekta ya uchukuzi na biashara, ikiwemo Kamati ya Maboresho ya Bandari ya Dar es Salaam ambayo hujadili namna ya kuboresha ufanisi wa bandari na kutatua changamoto za usafirishaji.

Alisisitiza kuwa sekta ya uchukuzi ndiyo uti wa mgongo wa uchumi wa Tanzania, huku akiielezea Tanzania kuwa lango muhimu la biashara kwa zaidi ya nchi nane za Afrika Mashariki, Kusini na Kati kutokana na nafasi yake ya kimkakati.

Magombana amesema bandari za Tanzania zilihudumia tani milioni 19.9 za shehena kati ya Julai na Desemba 2025. Serikali inatarajia kiasi hicho kuongezeka na kufikia zaidi ya tani milioni 40 ifikapo mwisho wa mwaka wa fedha 2025/26, kutoka tani milioni 32.75 zilizohudumiwa mwaka uliotangulia, na hivyo kuvuka lengo la kuhudumia tani milioni 30 ifikapo mwaka 2030/31.

Aidha, alisema awamu ya kwanza ya Kituo cha Lojistiki cha Kurasini chenye uwezo wa kuhudumia makasha 37,000 imekamilika, na kinatarajiwa kupunguza zaidi msongamano wa malori katika maeneo yanayozunguka Bandari ya Dar es Salaam.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa TRFA, Hussein Ahmad Wandwi, alisema chama hicho kilianzishwa mwaka 2022 na kusajiliwa rasmi Desemba 23, 2022 chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Alisema uanachama umeongezeka kutoka wanachama 15 mwaka 2022/23 hadi zaidi ya wanachama 550 mwaka 2024/25, jambo linaloonyesha imani kubwa ya wadau kwa chama hicho.

Wandwi alieleza kuwa dhamira ya TRFA ni kuwakilisha, kuwawezesha, kuwashauri na kufanya tafiti kwa niaba ya wasafirishaji wa mizigo kwa njia ya barabara nchini.

Aliongeza kuwa chama hicho kinalenga kujenga sekta ya usafirishaji iliyo salama, yenye ufanisi na kuaminika, ili kuchochea ukuaji wa uchumi na kupunguza gharama za usafirishaji huku kikihimiza uzingatiaji wa kanuni na sheria za Serikali.

Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mh.Riziki Pembe akikabidhi mfano wa hundi kwa Mshindi wa kwanza katika kipengele cha Riwaya cha Tuzo ya Safal ya Kiswahili ya Fasihi Afrika 2025 , Bw. Salim Hussein Ng’azi huku wageni wengine pamoja na viongozi wa Safal Group wakishuhudia. Hafla hiyo ilifanyika katika Chuo Kikuu Dar es Salaam mwishoni mwa wiki.

WASHINDI wa Tuzo ya Kiswahili ya Safal ya Fasihi ya Afrika wametangazwa leo katika shughuli iliyofana Jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mh. Paul Makonda ambaye aliwakilishwa na waziri mwenzake kutoka Zanzibar Mh. Riziki Pembe.

Waziri Makonda, katika hotuba yake, aliipongeza Kampuni ya Safal Group kupitia kampuni zake tanzu-Mabati Rolling Mills ya Kenya na ALAF Limited ya Tanzania kwa kudhamini tuzo hityo kwa miaka 10 sasa.

“Hii ni namna bora ya kukuza lugha ya Kiswahili hapa Tanzania na nchi za nje kama tunavyofahamu Kiswahili kwa sasa kinazungumzwa kote duniani ikiwemo nchi za ng’ambo ambako baadhi ya watanzania wameajiriwa ili wafundishe lugha hii,” alisisitiza.

Aliendelea kusema kuwa serikali itaendelea kutangaza lugha ya Kiswahili na kuhakikisha inatumika ipasavyo huku pia ikiandaa matukio mbalimbali yanayolenga matumizi ya lugha hii.

“Tutaendelea kufanya kazi kwa karibu na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na taasisi zingine zinazohimiza matumizi ya lugha hii ya Kiswahili,” alisema.

Aliwapongeza washindi wa mwaka huu na kuwahimiza kutumia vipaji vyao vya uandishi kujiendeleza na kuhakikisha pia wanajiingizia kipato kwa kuuza machapisho yao duniani kote.

Washindi wa mwaka huu ni:
Riwaya:
1. Salim Hussein Ng’azi (TZ) – Mwanamkasi ndio basi (5000USD)
2. Dickson Damas Mtalaze (TZ) – Shamba la mawe (2500 USD)

Ushairi:
1. Ali Hilal Ali (TZ) – Diwani ya vizikwa ya kale (5000USD)
2. Leonard Barnaba Mtesigwa (TZ) – Rima la miiko la balaa (2500 USD)

Hadithi Fupi:
1. Dominic Maina Oigo (KENYA) Mbunge mtarajiwa na hadithi nyingine (2500 USD)
Mwaka huu miswada 230 kutoka nchi saba ziliwasilishwa kwa majaji.
Afisa Mtendaji Mkuu wa ALAF Limited Bw. Bibhu Nanda alisema kampuni yake imedhamini tuzo hiyo kwa miaka 10 sasa kutokana na umuhimu wa lugha ya Kiswahili na jinsi imeendelea kuwaunganisha sio wakazi wa Afrika Mashariki tu bali watu tofauti duniani.

“Tukiwa tunaadhimisha miaka 10 tangu kuanzishwa kwa tuzo hii, tunapenda kuwashukuru wabia wetu wote ambao wamesimama na sisi katika kipindi hiki chote kwa lengo la kukuza na kutangaza lugha ya Kiswahili ambayo pamoja na mambo mengine imesaidia katika kurahisisha ufanyaji wa biashara katika ukanda huu,” alisema.

Tuzo ya Kiswahili ya Safal ya Fasihi ya Afrika ilianzishwa mwaka 2014 na Dkt. Lizzy Attree na Dkt. Mukoma wa Ngũgĩ ili kutambua kazi za uandishi katika lugha za Kiafrika sambamba na kuhamasisha kazi za utafsiri kwa lugha adhimu za asili ya Kiafrika.

Tuzo hiyo ambayo kwa mwaka huu inaadhimisha miaka 10 tangu kuanzishwa kwake mwaka 2015, imekuwa ikitolewa kila mwaka isipokuwa mwaka wa 2020, kutokana na kuweko janga la Covid 19 duniani kote.

Akiongelea tuzo hiyo, Dkt. Lizzy Attree amesema kwamba miaka 10 tangu kuanzishwa kwake ni hatua kubwa. Aliongeza, "Tayari tumeshatoa zaidi ya dola 150,000 kwa waandishi zaidi ya 40 mchango ambao umewawezesha kuchapisha zaidi ya vitabu 20. Ni matumaini yetu kuwa lugha zaidi za Kiafrika zitaendelea kutambuliwa kwa njia hii na kwamba kazi hii inaendelea kuikuza fasihi ya Kiswahili duniani".

Kwa upande wake Profesa Mukoma wa Ngũgĩ alielezea kuhusu mfumo wa uchapishaji unaohusiana na fasihi ya Kiswahili kwa kipindi cha mwongo mmoja, mfumo ambao amesema umeunganisha waandishi walioshinda tuzo mbalimbali moja kwa moja na wachapishaji wakiwemo Mkuki na Nyota na Mfuko wa Vitabu vya Ushairi wa Kiafrika (APBF).

Aliongeza, "Tunashukuru uongozi wa kampuni ya Safal, ambayo imetoa mchango mkubwa unaokuza tamaduni za Kiafrika. Tunatoa wito kwa serikali mbalimbali Barani Afrika, kupitia wizara zao za utamaduni kuunda mfumo ikolojia utakaohusisha lugha zote za Kiafrika".

Kwa mwaka huu, jumla ya kazi 230 kutoka mataifa saba ziliwasilishwa kwa ajili ya kuwania tuzo hizo

Akitangaza uamuzi wa Majaji kuhusiana na tuzo hizo, Mwenyekiti wa jopo la majaji wa tuzo kwa mwaka huu, Profesa Rayya Timammy kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi, alisema kuwa ushindani wa Tuzo ya Kiswahili ya Safal ya 2025 ya Fasihi ya Afrika ulikuwa mkubwa sana.

Alisema hali hiyo imesababishwa na idadi kubwa ya mawasilisho yaliyopokelewa kuwa na vipaji vya hali ya juu na kipekee vilivyoonyeshwa na waandishi waliowasilisha kazi zao hizo.

Profesa Timammy aliongeza, "Jopo la majaji lilikabiliwa na changamoto kubwa katika kuchagua washindi kwa sababu ya ubora wa kazi zilizowasilishwa. Bila shaka hii inaonyesha kwamba vipaji vya fasihi vinaendelea kukua na kushamiri kwa kasi ya ajabu".

Munyao Kilolo, Mkurugenzi wa Tuzo hiyo, alisema kwamba ukuaji huo umeendelea kukua kwa kipindi chote cha miaka 10 iliyopita. "Mwanzoni tulikuwa tukipokea mawasilisho chini ya 50 kwa mwaka, sasa hivi wanapokea mamia ya mawasilisho kila mwaka. na chini ya hati 50, na sasa tunapokea hati kwa mamia kila mwaka," alisema.

Kilolo alibainisha zaidi kwamba ukuaji huo umeenda sambamba kukua kwa jumuiya ya waandishi ambao mbali na wazo la uweko wa zawadi pia huwa wanashirikiana katika kukuza fasihi ya kiswahili.

Majaji wengine walioungana na Prof. Rayya Timammy katika kusoma na kuteua machapisho ambayo yatashiriki shindano la tuzo kwa mwaka wa 2025 walikuwa ni pamoja na Dkt. Masoud Mohammed wa Chuo Kikuu cha Zanzibar na aliyewahi kuwa mfanyakazi wa chuo kikuu cha Makerere Prof. Austin Bukenya.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Tuzo hii, Abdilatif Abdalla, aliongeza, “Ni jambo la kufurahisha mno kuona kwamba tangu mashindano yalipoanzishwa mwaka 2015, bado Tuzo hii inaendelea kuwavutia washiriki kutoka nchi mbalimbali na kwa idadi kubwa. Pia kiwango cha ubora wa miswada inayoshindanishwa kinaongezeka kila mwaka, na kwa hivyo kuitajirisha Fasihi ya Kiswahili.”

Mbali na zawadi hizo, machapisho yaliyoshinda pia yatapata fursa ya kuchapishwa kwa Kiswahili na kampuni ya uchapishaji ya Mkuki na Nyota iliyoko nchini Tanzania, ambapo mashairi yaliyoshinda yatatafsiriwa kwa lugha ya Kiingereza na kuchapishwa na Mfuko wa Vitabu vya Ushairi wa Kiafrika (APBF).

Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya eneo la Ngorongoro Abdul-Razaq Badru ameuambia mkutano wa 48 wa kamati ya Urithi wa Dunia kuwa Ngorongoro ni sehemu pekee ambayo binadamu duniani kote wanaweza kupata ushahidi sahihi wa chimbuko la asili ya binadamu.

Akizungumza mjini Busan,Jamhuri ya Korea wakati akiongoza Mkutano wa pembeni (Side event) ulioandaliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa lengo la kupata uelewa wa pamoja kuhusu hali ya uhifadhi wa eneo la  Hifadhi ya Ngorongoro ambayo ni eneo la Urithi wa Dunia, Badru amesema Ngorongoro ina ushahidi uliohifadhiwa wa nyayo za binadamu na masalia ya kale katika eneo la Laetoli na Olduvai zinazothibitisha suala hilo.

“Ngorongoro si tu eneo la utalii bali pia ni mahali ambapo historia ya binadamu wote kisayansi ilianzia”, alisema kamishna Badru.

Katika kikao hicho ameeleza kuwa kila nyayo iliyohifadhiwa ndani ya hifadhi ya Ngorongoro inawakumbusha kurudi nyumbani kuona historia hiyo.

Badru amefafanua  kuwa Ngorongoro ni sehemu ambayo binadamu alianzia kutumia zana mbalimbali za mawe kama teknolojia ya awali ya shughuli za kibinadamu na ndipo alipoanza kufanya harakati za kimaisha.

Mkutano wa kamati ya Urithi wa Dunia una lengo la kufanya maamuzi kuhusu maeneo mapya yanayopendekezwa kuingizwa kwenye Orodha ya Urithi wa Dunia na kuimarisha juhudi za pamoja za kulinda, kuhifadhi, na kusimamia kwa uendelevu maeneo yenye thamani kubwa ya kiutamaduni na asili duniani.




 ■ Waziri Mavunde ataka mnyororo wote wa utoroshaji wa madini hayo udhibitiwe,

■ Asikitishwa na upotevu wa mapato ya Serikali yatokanayo na vitendo hivyo,

■ Aelekeza wahusika wote wafutiwe leseni na kutoruhusiwa tena kufanya biashara ya madini,

■ Atoa rai kwa wananchi kufanya biashara ya madini kupitia mfumo rasmi


📍Dar es Salaam,

Kufuatia kuimarishwa kwa mfumo wa udhibiti wa biashara haramu ya madini unaofanywa na Wizara ya Madini kupitia Kikosi Kazi (Taskforce), madini aina ya dhahabu Gramu 4,402.20 yenye thamani ya 1,238,458,594.42 yamekatwa yakitoroshwa.

Hayo yamesemwa leo tarehe 27 Julai, 2026 na Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde (Mb) Jijini Dar es Salaam alipokuwa akizungumza na vyombo vya habari.

"Serikali kupitia Wizara ya Madini iliunda Kikosi kazi ambacho kinahusisha vyombo vya dola ili kudhibiti biashara haramu ya madini na utoroshaji. Hii ni sehemu tu ya kazi ambazo zimeendelea kufanywa na Kikosi kazi hicho katika kuimarisha mfumo wa ufanyaji biashara ya madini"

"Ndugu zangu, dhahabu hii yenye zaidi ya thamani ya bilioni 1.2 haikupitia katika mfumo rasmi wa ufanyaji biashara ya madini na hivyo kupelekea Serikali kukosa mapato ambayo yangeisaidia kuimarisha utoaji wa huduma mbalimbali kwa wananchi" Alisisitiza Mhe. Mavunde.

Aidha, Waziri Mavunde alibainisha kuwa dhahabu hiyo iliyokamatwa imetaifishwa kwa mujibu wa taratibu za Sheria na imehifadhiwa Benki Kuu ya Tanzania.

Vilevile, Mheshimiwa Mavunde amekielekeza Kikosi Kazi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya dola kumhoji vizuri mtuhumiwa aliyekamatwa na dhahabu hizo kufahamu alikotoka na alikuwa anapeleka wapi, ili kuweza kutibu kabisa mzizi wa vitendo hivyo na kuvunja mnyororo wa wote wa utoroshaji.

Mhe. Mavunde alisisitiza kuwa, iwapo mtuhumiwa aliyekamatwa alikuwa na leseni ya ufanyaji biashara ya madini kufutiwa leseni hiyo mara moja na kuingizwa kwenye orodha maalum ya wenye makosa (blacklisted) ili asiruhusiwe tena kufanya biashara ya madini nchini.

Katika hatua nyingine, Waziri Mavunde alitoa rai kwa wananchi wote kuzingatia na kufuata sheria na mifumo ya ufanyaji biashara ya madini ambayo tumejiwekea kupitia masoko ya madini na vituo vya ununuzi ambavyo vimesambaa Nchi nzima.






Top News