ZAIDI ya wananchi 8,000 kutoka Mkoa wa Arusha na maeneo mengine nchini wamepata huduma za uchunguzi na matibabu bila malipo katika siku mbili za kwanza za kambi maalumu ya afya inayofanyika jijini Arusha. Kambi hiyo ya siku saba ilianza Julai 13, 2026 na itahitimishwa Julai 19, ambapo wananchi wanapatiwa vipimo, ushauri wa madaktari bingwa, matibabu, dawa na rufaa bila malipo.

Kambi hiyo imeandaliwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha kwa kushirikiana na Ofisi ya Mbunge wa Arusha Mjini, Paul  Makonda, pamoja na Wizara ya Afya, hospitali za rufaa za kitaifa, taasisi maalumu za afya na hospitali binafsi. Katika siku ya kwanza wananchi 3,500 walihudumiwa, huku zaidi ya 4,500 wakipata huduma siku ya pili na kufanya jumla ya walionufaika kufikia zaidi ya 8,000.

Huduma zinazotolewa ni pamoja na vipimo mbalimbali vya afya, ushauri wa kitaalamu, matibabu, dawa na rufaa. Aidha, zaidi ya watu 50 walijitokeza kuchangia damu katika banda la Mpango wa Taifa wa Damu Salama, huku wagonjwa waliobainika kuhitaji matibabu ya kina wakipelekwa hospitalini kwa magari ya wagonjwa.

Akizungumza katika kambi hiyo, Makonda alimshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Wizara ya Afya, madaktari, taasisi za afya na sekta binafsi kwa kuwezesha huduma za kibingwa kuwafikia wananchi wa Arusha na maeneo ya jirani. Alisema mafanikio hayo yametokana na ushirikiano mzuri kati ya Serikali, viongozi wa wananchi, hospitali za rufaa na wadau wa sekta ya afya.

Makonda alisema wananchi wengi wanaofika kambini hawana uwezo wa kumudu gharama za vipimo na matibabu katika mazingira ya kawaida, huku baadhi wakishindwa kuendelea na matibabu baada ya fedha zao kuishia kwenye vipimo vya awali.

Alieleza kuwa ingawa wananchi wanapata huduma hizo bila malipo, taasisi, hospitali, madaktari na wadau wameingia gharama kubwa za usafiri, vifaa vya uchunguzi, dawa, miwani, malazi, chakula na mahitaji mengine muhimu ili kuhakikisha huduma zinawafikia wananchi.

Aliwasihi wananchi wanaopewa dawa, miwani na maelekezo ya matibabu kuyafuata kikamilifu, akisisitiza kuwa dawa na huduma zote zilizotolewa zimegharimiwa na hivyo ni muhimu zitumike ipasavyo ili kuleta matokeo yaliyokusudiwa.

Pia aliwahimiza wafanyabiashara, wamachinga, waendesha bodaboda na bajaji pamoja na wananchi wengine kutenga muda wa kupima afya, akisisitiza kuwa huduma hizo zinapatikana kwa watu wote bila kujali wanakotoka, dini, kabila, chama cha siasa au hali yao ya kiuchumi.





Na Peter Haule na Joseph Mahumi, WF, Tanga

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amesema Serikali itafuatilia kwa karibu changamoto zinazokwamisha utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa barabara ya Pangani-Tanga  ili kuhakikisha unakamilika kwa wakati na kuanza kutoa huduma kwa wananchi pamoja na kuchochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi.

Mhe. Balozi Omar alitoa kauli hiyo alipotembelea mradi wa ujenzi wa sehemu ya barabara ya Pangani mkoani Tanga yenye urefu wa kilometa 50 kwa kiwango cha lami, ambayo ni sehemu ya mradi mkubwa wa barabara ya Bagamoyo (Makurunge)–Saadani–Pangani yenye urefu wa kilometa 256.

Ziara hiyo inafuatia kilio cha uongozi wa mkoa na  Wilaya ya Tanga pamoja na wakazi wa Wilaya ya Tanga wanaoathirika na ubovu wa barabara hiyo unaokwamisha shughuli zao za kiuchumi hususan wakati wa mvua na masika.

Alisema mradi huo umechelewa kukamilika kwa muda mrefu, hali inayolazimu Serikali kuangalia kwa kina changamoto zinazouchelewesha ili kuhakikisha unakamilika na wananchi wanaanza kunufaika na huduma za usafiri na usafirishaji.

"Mradi huu ni muhimu kwa maendeleo ya wananchi na uchumi wa nchi. Tutafuatilia changamoto zinazoukabili ili utekelezaji wake ukamilike kwa wakati na uweze kutoa huduma iliyokusudiwa," alisema Mhe. Balozi Omar.

Kwa upande wake, Kaimu Meneja wa Wakala wa Barabara nchini-TANROADS Mkoa wa Tanga, Bw. Jotrevas August, alisema kuwa Mkandarasi anasuasua kukamilisha mradi licha ya juhudi za Serikali kuwataka watekeleze ujenzi wa mradi huo kwa wakati. 

Alisema kuwa mazungumzo yanaendelea kati ya Serikali na Mkandarasi huyo, ambaye ni Kampuni ya ujenzi ya CHICO kutoka China ili atafute rasilimali fedha kwa ajili ya kukamilisha mradi huo.

Alisema hadi sasa kazi mbalimbali zimeendelea vizuri, ikiwemo kusafisha eneo la barabara kwa urefu wa kilometa 44.45, sawa na asilimia 88.9 ya kazi hiyo. 

Aidha, ujenzi wa madaraja pamoja na matengenezo ya barabara ya awali na ya mchepuko kwa kiwango cha changarawe unaendelea sambamba na hatua nyingine za utekelezaji wa mradi.

Bw. August alisema kuwa mradi huo utakuwa kiungo muhimu kinachounganisha Bandari za Dar es Salaam, Tanga na Mombasa, hatua itakayoongeza ufanisi wa biashara na usafirishaji katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Mradi wa barabara ya Bagamoyo (Makurunge)-Saadani-Pangani unatarajiwa kuwa moja ya miundombinu muhimu ya kimkakati itakayorahisisha usafiri, kuimarisha biashara na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika ukanda wa pwani na nchi jirani za Afrika Mashariki.












Na Mwandishi wetu, Mirerani

KAMPUNI ya Franone Mining & Gem LTD imenufaisha jamii mbalimbali Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, kupitia miradi tofauti ya maendeleo ikiwemo ya sekta ya elimu, afya na miundombinu, kupitia uwajibikaji kwa jamii (CSR).

Meneja wa kampuni ya Franone Mining & Gem LTD, Sweetbert Arbogast ameeleza hayo kwenye ziara ya ujumbe wa shirika la Miss World ulipotembelea eneo la madini ya Tanzanite kitalu C mji mdogo wa Mirerani.

Ujumbe huo uliongozwa na Mwenyekiti na Mkurugenzi mtendaji wa shirika la Miss World, Julia Morley lenye makao makuu yake jijini London, Uingereza na mnyange Miss World Africa 2025 Hasset Dereje wa Ethiopia.

Arbogast ameeleza kuwa miradi hiyo iliyotekelezwa na Franone Mining kwa ajili ya kusaidia jamii imefanyika katika maeneo mbalimbali ya wilaya ya Simanjiro.

Ametaja baadhi ya mradi hiyo ni ujenzi wa zahanati kwenye migodi ya madini ya Tanzanite na ukarabati wa barabara ya kilomita nane inayopanda kwenye machimbo hayo.

"Pia Franone imetoa madawati 100 kwa shule ya sekondari Mirerani B.W.Mkapa, ujenzi wa miundombinu ya madarasa shule ya sekondari Naisinyai na ujenzi wa miundombinu ya kituo cha afya Mirerani," amesema Arbogast.

Ameeleza kuwa kwenye kipindi cha mafuriko yaliyotokea mwaka 2024 walitoa msaada wa chakula kwenye Tarafa ya Moipo na Kata ya Msitu wa Tembo na wanafunzi wa shule ya msingi Oloshonyokie.

Ofisa madini mkazi Mirerani (RMO) George Kaseza amesema eneo tengefu la Mirerani kuna vitalu mbalimbali vinavyochimbwa madini ya vito ya Tanzanite.

Kaseza ameeleza kwamba sehemu hiyo ina maeneo tofauti ambapo kuna kitalu A, B, C na D ambapo wachimbaji wenye migodi wamepewa leseni za kuchimba madini ya Tanzanite.

Katibu wa chama cha wachimbaji madini mkoa wa Manyara (MAREMA) Tawi la Mirerani Rachel Njau amesema ugeni huo ni mzuri kwao kwani utatumika kutangazwa zaidi kwa madini hayo ya vito ya Tanzanite kimataifa.

Mwenyekiti wa wanawake wafanyabiashara wa magonga, Magreth Sogweda, amesema wamepata faraja kutembelewa na ugeni huo kwani wameongezewa nguvu na moyo zaidi wa kazi wanazozifanya zinazidi kuthaminiwa.

Mwenyekiti wa chama cha wafanyabiashara wa madini mkoa wa Manyara, (Magebomita) Mokia Ole Mrefu amesema ugeni huo ni wakimataifa hivyo ni fursa nzuri kwa madini ya Tanzanite kuzidi kutangazwa na kufahamika zaidi.


-MACHAFUKO YATAZALISHA WALEMAVU WENGI ZAIDI"


Na Mashaka Mhando, TANGA.

SERIKALI imewatahadharisha Watanzania kuepuka vitendo vyovyote vinavyoweza kusababisha uvunjifu wa amani nchini, ikionya kuwa machafuko na kutovumiliana kisiasa ndio chanzo kikuu cha kuzalisha idadi kubwa ya watu wenye ulemavu.

Tahadhari hiyo nzito imetolewa jana jijini Tanga na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar, alipokuwa mgeni rasmi katika hafla kubwa ya ugawaji wa vifaa saidizi vilivyogharimu zaidi ya Shilingi Milioni 170 kwa watu wenye ulemavu; hafla iliyoandaliwa na Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Tanga, Mhandisi Mwanaisha Ulenge.

Akizungumza mbele ya mamia ya wakazi wa Jiji la Tanga, Waziri Omar alisisitiza kuwa wananchi wanapaswa kujenga utamaduni wa kutofautiana kwa mawazo bila kuhitilafiana kimatendo, kwani amani ndio msingi pekee wa maendeleo na ustawi wa jamii.

"Niwaombe tuendelee kudumisha amani yetu. Inapovunjika amani, wanaweza kupatikana walemavu wengi sana katika jamii. Tunaweza kutofautiana kwa mawazo, lakini isiwe sababu ya kuhitilafiana na kuvunja amani yetu," alionya Balozi Omar.

Pamoja na onyo hilo, Waziri Omar alitumia wasaa huo kumwagia sifa Mhandisi Ulenge kwa hatua yake ya kiungwana ya kuifikiria na kuigusa jamii ya watu wenye ulemavu, akieleza kuwa msaada huo unaimarisha utu wao na kuwapa fursa ya kuishi kwa kujitegemea na kuondokana na hofu ya kimaisha.


Mamilioni ya Vifaa Saidizi na Mafunzo ya PPRA

Awali, akisoma risala yake kwa mgeni rasmi, Mhandisi Mwanaisha Ulenge alibainisha kuwa vifaa hivyo vyenye thamani ya mamilioni ya fedha vimetolewa kupitia ufadhili wa Taasisi ya Kamal Foundation.


Alivitaja vifaa vilivyogawiwa kuwa ni pamoja na:

* Viti mwendo (Wheelchairs): 31

* Miguu bandia: 100

* Fimbo za wasioona: 25

Mhandisi Ulenge alifafanua kuwa, ili kuhakikisha walemavu hao hawabaki nyuma kiuchumi, walipatiwa pia elimu maalum ya manunuzi ya umma kupitia Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA). Hatua hiyo inalenga kuwawezesha makundi hayo maalum kushiriki kikamilifu katika fursa za kiuchumi na kupata tenda za Serikali ili kuongeza tija kwenye kazi zao.

Aidha, Mbunge huyo alitumia jukwaa hilo kuiomba Serikali kupitia Waziri wa Fedha kuharakisha upatikanaji wa fedha kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa miradi ya kimkakati mkoani humo, akiangazia zaidi umuhimu wa barabara ya Tanga–Pangani.

Vigogo wa CCM Watoa Neno

Akizungumza katika hafla hiyo, Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Tanga, Meja (Mst) Hamisi Mkoba, alieleza kuwa msaada huo mkubwa uliotolewa na Mbunge huyo ni sadaka yenye thamani kubwa isiyopimika.

"Haya yote tunayoyafanya leo ni kwa sababu nchi ina amani. Tuendelee kudumisha amani yetu. Hii ndiyo sadaka bora duniani," alisisitiza Meja Mstaafu Mkoba.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa UWT Mkoa wa Tanga, Hajat Sheymar Kweigir, alihitimisha kwa kueleza kuwa hatua iliyochukuliwa na Mhandisi Ulenge inaakisi kwa vitendo maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye amekuwa mstari wa mbele kuhakikisha makundi yenye mahitaji maalum nchini yanapata huduma bora na fursa stahiki.








Na Mwandishi wetu, Mirerani 

MWENGE wa uhuru umeweka jiwe la msingi kwenye wodi ya wanawake na watoto katika kituo cha afya Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, iliyojengwa na kampuni ya Chusa Mining LTD.

Kampuni ya Chusa Mining LTD chini ya Mkurugenzi wake Joseph Damasi Mwakipesile imejenga wodi hiyo ya wanawake na watoto kwa gharama ya shilingi milioni 230 kupitia mchango wao kwa jamii (CSR).

Kiongozi wa mbio za mwenye wa uhuru kitaifa mwaka 2026 Wazo Mwang'onda ameipongeza Chusa Mining LTD kwa kujenga wodi hiyo ambayo wanawake na watoto watalazwa na kupata huduma za afya katika kituo hicho cha afya pindi wakiugua.

Amesema mdau huyo wa maendeleo amejenga jengo hilo kutokana na jitihada za dhati za Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu kuweka mazingira rafiki kwa wachimbaji kufanya kazi, nao kutoa kiasi kwa jamii.

"Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya kwa sisi wakristo tunaamini kuwa Mungu anakujaribu pale unapotoa kwani amesema nijaribuni kupitia majitoleo na atakubariki pale ulipotoa hongera sana mdau wa maendeleo kwa kujitolea," amesema Mwang'onda.

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, James Ole Millya ambaye pia ni Mbunge wa Simanjiro amesema hatua ya Chusa Mining LTD kuwjenga wodi hiyo ni maendeleo makubwa.

Ole Millya amesema Chusa Mining wamekuwa msaada mkubwa kwa jamii kwani wanakwenda kumaliza changamoto ya upungufu ya wodi ya kulaza wanawake na watoto.

Mkurugenzi wa kampuni ya Chusa Mining LTD, Joseph Mwakipesile ametoa shukrani kwa Serikali kupitia Wizara ya Madini kwa namna wanavyotoa ushirikiano katika kazi zao.

Mwakipesile amesema wamejenga jengo hilo baada ya kusikia changamoto ya wodi ya wanawake na watoto ili kurudisha kidogo wanachokipata kwa jamii.

"Tunashukuru leo hii mwenge wa uhuru umeweka jiwe la msingi kwenye mradi huu wa wodi ya wanawake na watoto katika kituo cha afya Mirerani," amesema Mwakipesile.

Mganga mfawidhi wa kituo cha afya Mirerani Dkt Namnyaki Lukumay akisoma taarifa ya mradi huo amesema umegharimu shilingi milioni 230 na kujengwa na kampuni ya Chusa mining LTD.

Dkt Namnyaki amesema lengo kuu la mradi huo ni kuboresha upatikanaji wa huduma bora na rafiki za afya kwa wanawake na watoto na kuboresha afya ya familia na jamii kwa ujumla.

Amesema mradi huo ukikamilika utahudumia wanawake 5,000 na watoto zaidi ya 7,000 kwa mwaka katika kituo cha afya cha Mirerani.

"Sisi wananchi wa Simanjiro tunaishukuru Serikali ya awamu inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuboresha huduma za afya, kwa heshima na taadhima tunaomba utembee, kukagua na kuweka jiwe la msingi mradi wetu wa jengo la msingi mradi wetu wa jengo la wodi ya wanawake na watoto katika kituo cha afya Mirerani," amesema. 



Na Mwandishi wetu, Babati

NAIBU Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Regina Ndege amekabidhi mifuko 100 ya saruji kwa ajili ya ujenzi wa uzio wa hospitali ya Dareda Mission ya wilaya ya Babati mkoani Manyara, yenye ukosefu wa uzio, hali iliyokuwa ikihatarisha usalama wa wagonjwa na mali za hospitali.

Hatua hiyo imekuja kufuatia changamoto hiyo, ambapo Naibu Waziri Ndege aliahidi kuhakikisha uzio wa hospitali hiyo unajengwa kwa haraka ili kuboresha mazingira ya utoaji wa huduma za afya na kuongeza usalama kwa wagonjwa, watumishi na jamii wanaofika kupata huduma.

Naibu Waziri Ndege amesema huo ni utekelezaji wa ahadi aliyoitoa kwa uongozi na watumishi wa hospitali kwenye maadhimisho ya siku ya wafanyakazi duniani (Mei Mosi) mwaka huu, baada ya kubaini ukosefu wa uzio ulikuwa miongoni mwa changamoto kubwa zinazoikabili hospitali hiyo.

"Serikali itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuboresha huduma za afya nchini ili kuhakikisha wananchi wanahudumiwa vyema katika mazingira salama na rafiki," amesema Naibu Waziri Ndege.

Amesisitiza wadau pamoja na wananchi kuendelea kusimamia ipasavyo miradi yote inayotekelezwa na serikali ili ijengwe kwa viwango vinavyotakiwa na kuhakikisha thamani ya fedha zinazotolewa na serikali.

Ameeleza kuwa kuboresha miundombinu ya hospitali ni sehemu ya jitihada za kuhakikisha mazingira ya utoaji wa huduma za afya yanakuwa bora, salama na yenye kukidhi mahitaji ya watu.

Pia, Naibu Waziri Ndege amewahakikishia viongozi wa hospitali ya Dareda Mission kuwa ataendelea kushirikiana nao katika kuboresha miundombinu ya hospitali hiyo kwa maslahi ya jamii.

Mkurugenzi wa hospitali ya Dareda Mission, Padri Peter Salaho, ameishukuru serikali kwa mchango huo mkubwa, akisema utasaidia kuimarisha usalama wa hospitali na kuboresha mazingira ya utoaji wa huduma zake.

"Tunakushukuru sana Naibu Waziri Ndege, kwani ulipotembelea hospitali yetu tulikueleza changamoto ya ukosefu wa uzio na ulituahidi kutusaidia, sasa umetimiza ahadi yako," amesema Padri Salaho.

Diwani wa kata ya Dareda, Willbrod Bayo amempongeza na kumshukuru Naibu Waziri Ndege kwa kutimiza ahadi yake ya kutoa mifuko 100 ya saruji kwa ajili ya ujenzi wa uzio wa hospitali hiyo.

"Mara zote Naibu Waziri Ndege umekuwa msaada mkubwa kwa jamii, taasisi binafsi, za umma na mashirika ya kidini, tunakushukuru mno kwa kujitolea kwako kila wakati ukiitwa unaitika," amesema Bayo.

Mkazi wa Dareda kati Aloyce Tluway amempongeza Naibu Waziri Ndege kwa kutoa mifuko hiyo ya saruji ili kujenga ukuta kwani hospitali hiyo inaheshima kubwa kwa jamii ya eneo hilo.

"Hospitali ya Dareda Mission ni kongwe, watu wengi wamepata huduma hapo wengine wamezaliiwa hapo, wapo waliotibiwa maleria au kufanyiwa upasuaji hivyo Naibu Waziri Ndege amefanya jambo jema sawa na kulipa wema kwa jamii," amesema Tluway.



WANANCHI Watakiwa kujikita zaidi katika Kusoma na Kujifunza zaidi Elimu ya Usalama Barabarani ili kuepuka ajali zisizo za lazima hususani kwa Watoto Mashuleni.

Akizungumza na Wanahabari Jijini Dar es Salaam Mkurugenzi kutoka Chama cha  Mbio za Magari (AAT) Najma Rashid amesema kuwa Chama hicho kwa kushirikiana na  shirikisho la mbio za Magari duniani (FIA) kumekuwa na ushirikiano mzuri na wakaribu zaidi ili kuhakikisha programu ya mafunzo kwa ajili ya madereva pamoja na

watoto wa shule za sekondari na Misingi na wananufaika na Elimu ya Usalama barabarani ikiwemo kuzifahamu Alama za Barabarani, na Kuhakikisha wanarekebisha Miundombinu Barabarani (vivuko).

Hata hivyo amesema Mafunzo hayo yalianza mapema mwaka jana 2025 katika shule zilizopo Wilaya ya Kinondoni na hatimae kwa sasa ni Wilaya ya Ubongo na kusogea Wilaya ya Temeke Kwa Mwakani.

Pia ameeleza kuwa mwitikio umekuwa mkubwa zaidi kutokana na kupungua kwa ajali kwa watoto mashuleni na kwa Karibu wamekuwa wakipewa ushirikiano mkubwa na Askari wa Usalama Barabarani ambao ndio Wakufunzi katika Shule hizo.

Kwa Upande wa Mkufunzi wa programu hiyo ya Usalama Barabarani Askari sajenti Letcia Ishengoma kutokea traffic Makao Makuu amesema wamekuwa wakiendelea kutoa Elimu kila kona ikiwemo mashuleni,vijiwe vya bodaboda,stendi za mabasi ambapo tunatoa elimu ili watu waweze kubaini makosa kabla ya kutoa hukumu au adhabu ikiwemo faini na mengineyo pamoja na namna sahihi ya kutumia Alama za Barabarani.

Aidha amesema kuwa Jeshi la polisi litaendelea kutoa elimu ni Jambo endelevu ili kudhibiti tatizo mapema kabla ajali haijatokea hivyo programu hii inawanufaisha Wanafunzi Mashuleni ili kuwajengea uwezo wa kujua Alama za Barabarani na Kunusuru Ajali na vifo.




MKUTANO wa kikanda unaolenga kuimarisha mifumo ya tahadhari za mapema na huduma za hali ya hewa kwa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika umefunguliwa rasmi leo tarehe 13 Julai 2026 jijini Arusha.

Mkutano huu unawakutanisha wataalamu wa hali ya hewa na wadau kutoka nchi mbalimbali katika Bara la Afrika kujadili na kuweka mikakati ya kuimarisha utoaji wa tahadhari za matukio ya hali mbaya ya hewa na kuimarisha huduma za hali ya hewa kwa ujumla. Baadhi ya Nchi zinazo shiriki ni pamoja na Tanzania, Kenya, Misri, Angola, Madagascar, Afrika Kusini n.k.

Mkutano huo umeandaliwa kwa ushirikiano wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Ofisi ya Hali ya Hewa ya Uingereza (UK Met Office) na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA).

Katika hotuba yake ya ufunguzi, Dkt. Ladislaus Chang'a, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kitaifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa naTabianchi (IPCC), alisisitiza umuhimu wa kuimarisha usambazaji na uzingatiaji wa taarifa za utabiri na tahadhari. Vile vile, alibainisha kuwa, Mkutano wa 20 wa Baraza la Sekta ya Uchukuzi, Mawasiliano na Hali ya Hewa kwa Afrika Mashariki ulipitisha mapendekezo ya kuimarisha Taasisi za Kitaifa za Hali ya Hewa na kuchukua hatua stahiki ili kupunguza athari zinazoweza kusababishwa na El Nino 2026.

Kwa upande wake, Dkt. Agnes Kijazi, Mkurugenzi wa Ofisi ya Kanda ya Afrika ya WMO, alisisitiza kuwa hali ya hewa haina mipaka, na hivyo ushirikiano wa kimataifa ni muhimu sana. Alifafanua kuwa mkutano huo unalenga kuimarisha uratibu kati ya taasisi za kikanda ikiwemo Vituo Maalum vya Hali ya Hewa vya Kikanda ili kuongeza uwezo wao wa kusaidia Wanachama wa WMO katika kutoa huduma za hali ya hewa. "Hili ni jukumu kubwa ambalo haliwezi kutekelezwa bila kukuza ushirikiano wa kimataifa," alisisitiza Dkt. Kijazi.

Naye, Fionne Marshall, Kiongozi wa Kanda ya Afrika kutoka Ofisi ya Hali ya Hewa ya Uingereza, alitoa wito wa utabiri na tahadhari kuwa sahihi, zenye kuaminika, na zenye kutoa hatua stahiki zakuchukuliwa. "Haitoshi kujua kwamba mvua kubwa inakuja ikiwa watu hawaelewi athari kubwa zinaweza kutokea. "Haitoshi kutoa tahadhari ikiwa jamii hazipati, haziiamini, au hazijui hatua ya kuchukua," alisema Marshall, akiwataka taasisi kufanya kazi kwa mwelekeo mmoja wa kuelewa athari.

Wawakilishi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Kamisheni ya Umoja wa Afrika (AUC) walithibitisha majukumu yao katika kuimarisha mifumo ya tahadhari za mapema, huku James Kivuva wa EAC akibainisha kuwa uratibu bado ni pengo muhimu ambalo lazima lifanyiwe kazi na lifungwe. Naye, Dkt. Jolly Wasambo wa AUC alisisitiza dhamira ya bara kama ilivyoainishwa katika Agenda 2063, akisisitiza kwamba hali ya joto duniani inavyoendelea kuongezeka ndivyo ulazima wa kuimarisha mifumo ya tahadhari mapema unavyohitajika kwaajili ya jamii salama.

Kuanzia tarehe 13 hadi 17, washiriki watajadili namna ya kuimarisha vituo vya kikanda, kuimarisha Taasisi za Kitaifa za Hali ya Hewa, kuimarisha utabiri unaozingatia athari kwa ajili ya El Nino 2026, na kuimarisha ushirikiano katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT) na Akili Unde.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali itaendelea kuimarisha ushirikiano na Benki ya CRDB katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya maendeleo Zanzibar.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 14 Julai 2026, alipokutana na uongozi pamoja na wajumbe wa Bodi ya Benki ya CRDB, waliofika Ikulu Zanzibar kwa mazungumzo.

Amesema Serikali inathamini mchango wa benki hiyo katika kufanikisha miradi mbalimbali ya maendeleo na itaendelea kufanya kazi kwa karibu katika ujenzi wa skuli, nyumba za makaazi, miradi ya kilimo na kuwezesha upatikanaji wa mikopo kwa wananchi.

Aidha, ameipongeza CRDB kwa kutoa mikopo kwa wajasiriamali wadogo na wa kati, kuwajengea uwezo watendaji wa sekta ya umma na kuisaidia Serikali kupata mikopo kutoka taasisi za fedha za kimataifa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya CRDB, Prof. Neema Munisi Mori, amesema benki hiyo itaendelea kushirikiana na Serikali katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo na programu za kuwawezesha vijana, wanawake na wajasiriamali.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB, Dkt. Abdulmajid Mussa Nsekela, ameipongeza Serikali kwa maendeleo yaliyofikiwa na kuanzishwa kwa akaunti maalum ya kulipa madeni ya mikopo ya miradi ya kimkakati, hatua iliyoongeza ufanisi na kuimarisha imani ya taasisi za fedha kwa Serikali.
















Balozi wa Tanzania nchini China, Dkt. Suleiman Haji, akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo Julai 14, 2026.
Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA), Gilead Teri akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo Julai 14, 2026.

Na Mwandishi Wetu
WAKATI uhusiano wa kibiashara kati ya Tanzania na China ukiendelea kuimarika, Balozi wa Tanzania nchini China, Dkt. Suleiman Haji, amesema tathmini ya ushiriki wa Ubalozi wa Tanzania katika Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) imeibua mkakati wa kuwasaidia Watanzania kutumia fursa za biashara na uwekezaji katika soko la China.

Akizungumza na waandishi wa habari leo, Julai 14, 2026, Dkt. Haji alisema takribani Watanzania 500 walitembelea banda la ubalozi huo na kubaini changamoto mbalimbali zinazowakabili wafanyabiashara wanaotaka kufanya biashara za kimataifa.

Alisema changamoto hizo ni pamoja na uzalishaji hafifu usiokidhi viwango vya kimataifa, uelewa mdogo wa taratibu za biashara za kimataifa, pamoja na udhaifu wa vifungashio unaopunguza ushindani na thamani ya bidhaa za Tanzania katika masoko ya nje.

Aidha, alisema wafanyabiashara wengi walieleza kuwa baadhi ya taasisi zinazopaswa kuwawezesha kushiriki katika biashara za kimataifa zimekuwa zikikwamisha juhudi zao badala ya kuzisaidia.

Dkt. Haji alisema Tanzania ina fursa kubwa za kushirikiana na China katika sekta za kilimo, uvuvi, nishati na madini, huku akibainisha kuwa idadi ya watalii kutoka China wanaotembelea Tanzania imefikia takribani 82,000 na inatarajiwa kufikia 100,000 mwaka ujao.

Kutokana na changamoto zilizobainika, alipendekeza kuanzishwa kwa Kliniki ya Biashara itakayotoa elimu na ushauri kuhusu biashara za kimataifa, kuboreshwa kwa utekelezaji wa sera ya ushuru sifuri, kuimarishwa kwa elimu kuhusu fursa zilizopo China na masoko mengine, pamoja na kuanzishwa kwa kituo kimoja kitakachounganisha taasisi zote zinazoshughulikia biashara za kimataifa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA), Gilead Teri, alimpongeza Dk. Haji kwa kuanzisha zoezi hilo, akisema litakuwa na mchango mkubwa katika kuongeza ushiriki wa Watanzania katika biashara za kimataifa na kuvutia uwekezaji nchini.




Na Mwandishi Wetu
MAMLAKA ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) imeibuka mshindi wa kwanza katika kundi la Taasisi za Udhibiti kutokana na utoaji bora wa elimu kwa wananchi katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) 2026.

Akizungumza mara baada ya kupokea tuzo hiyo, Meneja wa PPRA Kanda ya Pwani, Vicky Mollel, alisema ushindi huo ni heshima kubwa kwa mamlaka hiyo na umetokana na imani na ushirikiano mkubwa waliooneshwa na Watanzania waliotembelea banda la PPRA wakati wa maonesho hayo.

Alisema PPRA itaendelea kuboresha huduma zake ili kuhakikisha wananchi wanapata elimu na huduma za ununuzi wa umma kwa viwango vya juu, sambamba na kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa.

"Ushindi huu ni heshima kwa PPRA na unatupa nguvu ya kuendelea kuwahudumia Watanzania kwa ufanisi zaidi. Tunaendelea kujizatiti kuhakikisha huduma zetu zinabaki kuwa bora wakati wote," alisema Mollel.

Alibainisha kuwa katika kipindi chote cha maonesho, wananchi wengi walifika kwenye banda la PPRA kupata elimu kuhusu mfumo wa kielektroniki wa ununuzi wa umma (NeST), huku idadi kubwa wakijisajili ili kushiriki katika zabuni na fursa mbalimbali za ununuzi wa umma.

Mollel alisema mwitikio huo unaonesha kuongezeka kwa uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa kushiriki katika ununuzi wa umma kwa kutumia mifumo ya kidijitali, jambo linalochangia uwazi, ushindani na uwajibikaji katika matumizi ya fedha za umma.

Alisisitiza kuwa PPRA itaendelea kutoa elimu kwa wadau na wananchi nchini kote ili kuongeza ushiriki wa Watanzania katika fursa za ununuzi wa umma, huku ikihakikisha shughuli zote zinaendeshwa kwa kuzingatia sheria na taratibu zinazotawala sekta hiyo.

Top News