Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Idara ya Mambo ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa (SUKI), Ndugu Rabia Abdalla Hamid (MCC), amewasisitiza wananchi wa Mkoa wa Pwani kuendelea kulinda amani, utulivu na mshikamano wa Taifa, akieleza kuwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kitaendelea kusimamia jitihada za kuboresha na kustawisha maisha ya kila Mtanzania.

Ndugu Rabia amesema kila Mtanzania ni sehemu ya historia na maendeleo ya Tanzania, hivyo ana wajibu wa kulinda amani, umoja na utulivu wa nchi kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Ametoa kauli hiyo leo, Agosti 23, 2026, wakati akiendelea na ziara yake katika Mkoa wa Pwani yenye lengo la kusikiliza makundi mbalimbali ya kijamii, kubaini changamoto zinazowakabili na kutafuta namna bora ya kuzitatua.

Katika ziara hiyo, Ndugu Rabia amekutana na kuzungumza na makundi mbalimbali, yakiwemo viongozi wa dini, wazee, wakulima, wafugaji, mashirika yasiyo ya kiserikali (NGOs), umoja wa wasusi, wafanyabiashara, wanamichezo, wavuvi, wanavyuo, walimu, Machinga, Mawinga, Mama Lishe, Baba Lishe, vyama vya ushirika, umoja wa mashamba ya chumvi, wajane, wachimbaji wa madini, maafisa usafirishaji pamoja na vikundi mbalimbali vya ujasiriamali.

Amesema CCM itaendelea kusikiliza wananchi na kufuatilia changamoto zao kwa lengo la kuhakikisha jitihada za maendeleo zinagusa makundi mbalimbali na kuboresha maisha ya wananchi.

Ndugu Rabia amesisitiza kuwa ushirikiano kati ya wananchi na Serikali ni muhimu katika kujenga Tanzania yenye amani, umoja na maendeleo endelevu.
















Na Hassan Kimweri, WAF – Addis Ababa

Tanzania imesisitiza umuhimu wa Afrika kuwa na sauti moja, uongozi madhubuti na uwakilishi wenye nguvu katika maamuzi ya afya duniani ili kuhakikisha maslahi na vipaumbele vya Bara hilo vinapewa uzito katika mchakato wa mageuzi ya Muundo wa Mfumo wa Afya Duniani (Global Health Architecture – GHA).

Naibu Waziri wa Afya Mhe. Dkt. Florence Samizi amesema hayo leo Agosti 23, 2026 jijini Addis Ababa, Ethiopia, alipomwakilisha Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa katika Kikao cha 'African High-Level Ministerial Committee' kuelekea Mkutano wa 76 wa Kamati ya Kanda ya Afrika ya Shirika la Afya Duniani (WHO AFRO RC76).

"Tanzania inaunga mkono kikamilifu mchakato wa mageuzi ya GHA na kuipongeza Africa CDC kwa kuteuliwa kuwa Taasisi ya kikanda ya afya katika mchakato huo, hatua hii ni fursa kwa Afrika kushiriki kikamilifu katika kuamua mwelekeo wa mfumo wa afya duniani," amesema Dkt. Samizi

Akizungumzia umuhimu wa mageuzi hayo kwa wananchi, Dkt. Samizi amesema mfumo wa afya duniani unapaswa kuzingatia mahitaji halisi ya nchi, ikiwemo upatikanaji wa fedha, teknolojia na uwezo wa kukabiliana na milipuko ya magonjwa.

"Dunia kwa sasa inakabiliwa na changamoto za upatikanaji wa fedha za afya, mabadiliko ya kijiografia na kisiasa pamoja na majadiliano kuhusu mkataba wa Kimataifa wa kukabiliana na milipuko ya magonjwa, upatikanaji wa vimelea na mgawanyo wa manufaa (PABS)," amesema Dkt. Samizi

Aidha, Dkt. Samizi amesema mfumo mpya wa afya duniani unapaswa kuwa na mgawanyo wa majukumu ulio wazi kati ya taasisi za kimataifa, kikanda na kitaifa, kupunguza urudiaji wa majukumu na kuhakikisha fedha zinaelekezwa katika vipaumbele vya nchi.

Kwa upande wa hatua zinazofuata, Dkt. Samizi amezihimiza nchi wanachama kushiriki kikamilifu katika mashauriano ya kila mwezi kuhusu mageuzi ya GHA, huku akipendekeza Afrika CDC na WHO AFRO ziwakutanishe Mawaziri wa Afya wa Afrika ifikapo Novemba 2026, baada ya kukamilika kwa rasimu ya kwanza ya ripoti ya "GHA Joint Task Force", ili kupitia mapendekezo na kutoa mwongozo wa kisiasa.

Akihitimisha hotuba yake Dkt. Samizi amesema Tanzania inaendelea kutoa ushirikiano katika kujenga mfumo wa afya duniani wenye usawa, unaowajibika, unaoitikia mahitaji kwa wakati na unaozingatia changamoto za nchi zinazoendelea.










Benki ya NMB imeendelea kuunga mkono jitihada za Serikali za kuimarisha afya ya mwili na akili ya watumishi kupitia Mashindano ya Kitaifa ya SHIMISEMITA yanayoendelea mkoani Mbeya.

Mashindano hayo yanawakutanisha zaidi ya watumishi 5,000 kutoka halmashauri 184 nchini, huku NMB ikiendelea kuwa miongoni mwa wadau wanaoyaunga mkono.

Meneja wa NMB Kanda ya Nyanda za Juu, Wogofya Mfalamagoha, alisema ushiriki wa benki hiyo unatokana na imani kwamba mtumishi mwenye afya ana nafasi kubwa ya kuwa na tija na kutoa huduma bora kwa wananchi. Katika mashindano ya mwaka huu, NMB imetoa Sh milioni 34.5 pamoja na jezi kwa timu zitakazofuzu hatua ya robo fainali katika mpira wa miguu, wavu, pete na kikapu.

Mgeni rasmi, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Prof. Riziki Shemdoe, aliyemwakilisha Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, aliipongeza NMB kwa kuendelea kushirikiana na Serikali katika shughuli zinazochangia ustawi wa watumishi na wananchi. Alisema michezo inasaidia kujenga umoja na mshikamano miongoni mwa watumishi wa serikali za mitaa.

Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Beno Malisa, alisema ujio wa maelfu ya washiriki wa SHIMISEMITA pia umeongeza shughuli za kiuchumi mkoani humo. Kupitia mashindano hayo, michezo inaendelea kuwa jukwaa la kuimarisha afya na ushirikiano wa watumishi huku Tanzania ikijiandaa kuwa mwenyeji mwenza wa AFCON 2027 pamoja na Kenya na Uganda.









Na Mwandishi wetu, Simanjiro

MDAU wa maendeleo wa Mkoa wa Manyara, Taiko Ole Kulunju ameongoza harambee ya ujenzi wa madarasa ya shule ya msingi Noomunyi kijiji cha Loiborsiret Wilayani Simanjiro na kupatikana shilingi milioni 71,050,000.

Taiko akizungumza kwenye harambee hiyo amewapongeza wakazi wa vitongoji vyote vya kijiji cha Loiborsiret kwa kujitoa kwa moyo mmoja katika kuchangia ujenzi wa madarasa ya shule mpya ya Noomunyi.

"Nawashukuru Diwani wa Kata yetu Mhe Ezekiel Lesenga Mardadi, mjomba wangu Edward Loure wa UCRT, Lamnyaki Lazaro na mgeni wetu Paulo kutoka Wilaya ya Monduli na watu wote wa Loiborsiret, kwa kutuunga mkono kwenye harambee hii," amesema Taiko.

Amesema kukamilika kwa madarasa ya shule hiyo itakuwa vyema kwa wanafunzi wa eneo hilo kusoma karibu kwani wanaotembea umbali mrefu kufuata elimu ya msingi.

"Nawashukuru Diwani wa Kata yetu Mhe Ezekiel Lesenga Mardadi, mjomba wangu Edward Loure wa UCRT, Lamnyaki Lazaro na mgeni wetu Paulo kutoka Wilaya ya Monduli na watu wote wa Loiborsiret, kwa kutuunga mkono kwenye harambee hii," amesema Taiko.

Diwani wa kata ya Loiborsiret Ezekiel Lesenga (Mardadi) amewapongeza wadau mbalimbali na wananchi wa eneo hilo kwa mchango wao.

Mardadi ameeleza kwamba ataishirikisha Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro ili nao wachangie ujenzi wa madarasa mengine ya shule hiyo mpya iliyojengwa kwa nguvu za jamii.

Mratibu wa shirika lisilo la kiserika la Ujamaa Community Resource Team (UCRT) Edward Loure amesema amefanikisha ujenzi wa madarasa mawili ya shule hiyo.

Loure ameiasa jamii ya eneo hilo kuweke juhudi kubwa katika kuzingatia elimu ya watoto wao na kutunza ardhi ambayo ni urithi wa eneo hilo.

"Kila wakati nimekuwa nikisema kuwa our land is our life (ardhi yetu ndiyo maisha yetu hivyo tuilinde ardhi yetu kwa manufaa ya watoto wetu na mifugo yetu," amesema Loure.




Na. Benny Mwaipaja, Dar es Salaam.

KAMPUNI ya kimataifa ya Fitch Rating inayojihusisha kufanya tathmini ya uwezo wa nchi kukopesheka katika masoko ya fedha ya Kimataifa. Katika tathmini yake Fitch imetoa alama ya B (Positive), katika kiwango cha B+, hatua inayodhihirisha kuimarika kwa misingi ya uchumi na uimara wa sera za uchumi jumla nchini.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo waliochapisha katika tovuti rasmi ya Kampuni hiyo, Fitch imesema mabadiliko hayo yanatokana na kuimarika kwa akiba ya fedha za kigeni, kuwepo kwa nakisi ya bajeti inayodhibitika na kuendelea kwa ukuaji wa uchumi, mambo ambayo kwa pamoja yanatarajiwa kuongeza mapato kusaidia kuhudumia bajeti ya nchi pamoja na kupunguza mzigo wa deni la Serikali.

Aidha, Fitch imesema akiba ya fedha za kigeni nchini inatarajiwa kuongezeka kutoka dola za Marekani bilioni 6.3 mwishoni mwa mwaka 2025 hadi kufikia dola bilioni 7.9 mwaka 2028, sawa na uwezo wa kugharamia malipo ya nje kwa takribani miezi 3.3.

Fitch imeeleza kuwa, kupungua kwa changamoto katika soko la fedha za kigeni na kuongezeka kwa unyumbufu wa kiwango cha ubadilishaji wa fedha kumechangia kupunguza baadhi ya hatari za muda mfupi, huku akiba ya dhahabu isiyo ya fedha inayomilikiwa na Benki Kuu ya Tanzania, inayokadiriwa kufikia dola bilioni 2.4, inaweza kuongeza zaidi kinga ya nchi dhidi ya mishtuko ya nje.

Katika upande wa bajeti na usimamizi wa deni, Fitch imekadiria kuwa nakisi ya bajeti kwa mwaka wa fedha ulioishia Juni 2026 ilikuwa asilimia 2.8 ya Pato la Taifa, ikichangiwa na ongezeko la ukusanyaji wa mapato na athari ndogo za ruzuku za mafuta katika utekelezaji wa bajeti na inatarajiwa nakisi hiyo kubaki karibu asilimia 3 ya Pato la Taifa hadi mwaka wa fedha 2028, likizingatia kuendelea kwa maboresho katika ukusanyaji wa mapato kupitia Mpango wa Muda wa Kati wa Mapato.

Fitch imebainisha kuwa mapato ya kodi yaliongezeka kutoka asilimia 14.6 hadi asilimia 15.6 ya Pato la Taifa kati ya Mwaka wa Fedha 2023 na Mwaka wa Fedha 2025.

Fitch pia imetabiri kuwa deni la Serikali kwa uwiano na Pato la Taifa litapungua kutoka asilimia 48.9 mwaka 2025 hadi asilimia 46.2 mwaka 2028, kiwango ambacho kitakuwa chini ya wastani wa asilimia 55 unaokadiriwa kwa nchi zilizo katika kundi la ukadiriaji wa B, na wameeleza kuwa kupungua kwa deni kutachangiwa na ukuaji mkubwa wa Pato la Taifa kwa thamani ya sasa pamoja na nakisi ndogo ya msingi ya bajeti.

Katika upande mwingine Fitch imepongeza hatua zinazochukuliwa kuboresha usimamizi wa fedha za umma, likibainisha kuwa hadi Machi 2026, kiasi cha madeni yaliyothibitishwa ya Serikali kwa wazabuni na marejesho ya kodi kilikuwa kimepungua hadi asilimia 0.2 ya Pato la Taifa kutoka asilimia 1.2 Desemba 2022.

Kwa upande wa ukuaji wa uchumi, Fitch inatarajia Tanzania kuendelea kufanya vizuri ikilinganishwa na wastani wa nchi zilizo katika kundi la B, ikitabiri ukuaji wa Pato la Taifa kwa asilimia 5.8 mwaka 2026, dhidi ya wastani wa asilimia 3.7 kwa kundi hilo, na uchumi unatarajiwa kukua kwa wastani wa asilimia 6.1 katika kipindi cha 2027–2028, ukichochewa na uwekezaji wa umma, utalii, nafasi ya Tanzania kama kitovu cha usafirishaji na biashara kikanda pamoja na ukuaji wa sekta ya madini.

Wakati huo huo, Fitch inatarajia mfumuko wa bei wa wastani wa asilimia 4.2 mwaka 2026, kutoka asilimia 3.3 mwaka 2025, lakini bado ukiwa chini ya wastani wa asilimia 5.6 unaotarajiwa kwa nchi za kundi la B.

Fitch imeeleza pia kuwa Tanzania imepiga hatua katika kuboresha mfumo wa sera za uchumi jumla tangu mwaka 2023, kupitia maboresho ya kitaasisi na kiutendaji yaliyoimarisha uhuru wa benki kuu, mfumo wa uendeshaji wa kiwango cha ubadilishaji wa fedha na usimamizi wa soko la fedha za kigeni.

Aidha, wameongeza kuwa maboresho hayo yanaweza kuongeza uwezo wa Tanzania kukabiliana na mishtuko ya kiuchumi, ingawa baadhi yake bado yanahitaji kuthibitishwa kupitia utekelezaji wake kwa muda, lakini pia wasiwasi wa awali kuhusu uwezo wa takwimu za kitaifa kuakisi mabadiliko ya ukuaji wa uchumi umepungua baada ya kukamilika kwa zoezi la kubadili mwaka wa msingi wa Pato la Taifa Juni 2026.

Fitch inatazamia kuendelea kuimarika kwa akiba ya fedha za kigeni, kuongezeka kwa ufanisi katika ukusanyaji wa mapato, udhibiti wa matumizi ya Serikali na kushuka kwa uwiano wa deni kwa Pato la Taifa ni miongoni mwa mambo yatakayoweza kuchangia hatua zaidi ya kuboresha ukadiriaji wa Tanzania. Shirika hilo limeeleza kuwa kuongezeka kwa imani kwamba maboresho ya mfumo wa sera za uchumi jumla yataendelea kuimarisha uwezo wa nchi kukabiliana na mishtuko ya nje na kudumisha utulivu wa uchumi kutakuwa msingi muhimu wa hatua hiyo.

Kwa ujumla, Fitch imeona mwenendo wa uchumi wa Tanzania ukiwa na msingi chanya, huku ikiweka mkazo katika kuendelezwa kwa nidhamu ya fedha, kuimarishwa kwa mapato ya ndani na utekelezaji endelevu wa maboresho ya sera ili kujenga mazingira imara zaidi ya uchumi.







NA MWANDISHI WETU


Historia kubwa imeandikwa Tanzania. Hii ni kufuatia kukamilika kwa mradi wa Kituo cha Kuzalisha Umeme cha Julius Nyerere (JNHPP), chenye uwezo wa kuzalisha megawati 2,115 katika eneo la mradi, wilayani Rufiji, mkoani Pwani.

Kukamilisha kwa mradi huo uliogharimu shilingi trilioni 7.452, kunachochea moja kwa moja maendeleo ya shughuli za kijamii na kiuchumi kupitia uzalishaji wa nishati ya umeme ambayo ni muhimu katika shughuli hizo.

Rais Dk. Samia Suluhu Hassan amezindua rasmi mradi huo Agosti 22, 2026 wilayani Rufiji.

Akitoa maoni yake kuhusiana na uzinduzi wa mradi huo, Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Taifa, Mary Chatanda, amesema kama Rais Dk. Samia asingekuwa thabiti katika uongozi wake, mradi huo usingekamilika.

"Rais Dk. Samia alipoingia madarakani mwaka 2021, alikuta mradi huu umefikia utekelezaji wa asilimia 33, lakini ndani ya miaka mitano ya uongozi wake, mradi huo umekamilika wote na unazalisha megawati 2,115 za umeme," amesema Chatanda.

Amebainisha kuwa, uzalishaji wa megawati hizo unaleta uhakika kwa nchi yetu kujitosheleza kimahitaji na kuwa na uwezo wa kuuza ziada ya umeme nje ya nchi, na kuongeza pato la nchi.

"Mradi huu umechangia asilimia 44.9 za umeme katika Gridi ya Taifa, na hivyo unamaliza kabisa mahitaji ya umeme yaliyopo nchini, na hivyo kuwezesha shughuli za viwanda, biashara, uwekezaji, kilimo, utoaji wa huduma bora za kijamii kama elimu, afya, maji kufanikiwa kupitia upatikanaji wa umeme wa uhakika," amesema.


AMPONGEZA RAIS SAMIA KUTIMIZA NDOTO ZA HAYATI MWALIMU JULIUS NYERERE

Mwenyekiti huyo UWT Taifa amesema, kuzinduliwa mradi huo, kunatimiza ndoto za zaidi ya miaka 50 za Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, aliyetamani mradi huo ukamilike.

"Agosti 22, 2026, inabaki siku ya kihistoria nchini kwani ndoto za Hayati Mwalimu Nyerere zimetimia. Hayati Dk. John Magufuli alifufua ndoto hizo, lakini mama yetu Dk. Samia amekamilisha, na sasa si ndoto tena bali ni kitu halisi," ameongeza.

Ikumbukwe kuwa, mradi huo una mitamboni tisa ya uzalishaji ambayo yote inafanya kazi. Aidha, Tanzania imeweka historia ya aina yake barani Afrika na ulimwenguni kwa kuwa na uhakika wa nishati ya umeme kwa mahitaji ya ndani na kuwa na ziara ya kuuza nje ya nchi.


Na Mashaka Mhando, Tanga

Hatimaye, Mzee Mohamed Rashid Mkwaje, ambaye aliondoka nyumbani kwao tangu mwaka 1974 kwenda kufanya kazi ya kukata mkonge wilayani Muheza, amefanikiwa kurejea na kuungana tena na familia yake katika Kijiji cha Ligunga, wilayani Tunduru mkoani Ruvuma, baada ya kupita miaka 52.

Mzee huyo amepokelewa kwa hisia kali na vilio vya furaha, hasa kutoka kwa mama yake mzazi, Asmin Kandulu ambaye alikuwa amekata tamaa na kutokuwa na uhakika kama mwanaye alikuwa bado hai baada ya ukimya wa zaidi ya nusu karne.

Kufuatia mapokezi hayo, wajukuu na ndugu wengine wa familia walimfanyia matambiko maalum ya kimila yaliyoambatana na nyimbo za asili za kabila la Kihiyao, ikiwa ni ishara ya kumpokea na kusherehekea kurejea kwa mtoto wao aliyekuwa amepotea.

Safari ya kurejea kwa Mzee Mkwaje ilianza Alhamisi Augosti 20 akitokea Wilaya ya Muheza mkoani Tanga, ambapo alisindikizwa na Ofisa Ustawi wa Jamii wa wilaya hiyo, Silvanus Misigaro.

Akizungumza baada ya kufanikisha safari hiyo, Misigaro alisema walimkabidhi mzee huyo kwa Mganga Mkuu wa Wilaya ya Tunduru Alfred Rwechungura pamoja na Ofisa Ustawi wa eneo hilo, ambao walishirikiana kumfikisha hadi kijijini kwao Ligunga.

"Alipokelewa na mama yake mzazi Asmina, kiukweli mama yake alilia sana kwa kumkosa mtoto wake kwa miaka mingi. Alikuwa na hisia sana na hakuwa na uhakika kama mwanaye huyu bado alikuwa hai," alisema Misigaro akisimulia tukio hilo la kusisimua.

Awali, Mzee huyo ambaye alikuwa akiishi Kijiji cha Ngomeni wilayani Muheza bila familia yoyote, alifika katika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Muheza kuomba msaada wa nauli ya kumrudisha kwao. Kufuatia maombi hayo, ofisi hiyo ilimpatia kibali maalum cha kuchangisha fedha za hiari (Kumb. Na. DC/MUH/S.20/VOL. VIII/232) kilichoanza kutumika Agosti 10 mwaka huu.

Hata hivyo, wakati Mzee Mkwaje akiwa amefanikiwa kuchangisha kiasi cha Shilingi 30,000 pekee kupitia kibali hicho, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Balozi Dkt. Batilda Burian, aliguswa na mkasa huo na kutoa msaada wa Shilingi 200,000 kwa ajili ya nauli, fedha zilizokabidhiwa kupitia kwa Mwandishi wa Habari, Mashaka Mhando, ambaye naye alimkabidhi Ofisa Ustawi, Misigaro.

Akizungumza kwa furaha baada ya kufika nyumbani na kuonana na wapendwa wake, Mzee Mkwaje alitoa shukrani za dhati kwa Serikali ya Wilaya ya Muheza na Tunduru, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, na watu wote waliojitolea kwa namna moja au nyingine kuhakikisha anatimiza ndoto ya kuonana tena na mama yake tangu alipoondoka kwenda kwenye mashamba ya mkonge miongo mitano iliyopita.

"Naishukuru serikali kusema kweli, wameniheshimisha, sikuwa nina uhakika kama kweli nitarudi nyumbani, niliona kama jambo ambalo haiwezekani kutokana na kwamba nilikuwa naona sieleweki ombi nililokuwa nataka kurudi nyumbani, nawashukuru wote waliohusika na hili," alisema.




-HAPI AKUTANA NA RAIS DANIEL CHAPO WA MSUMBIJI, AWASILISHA SALAMU ZA MWENYEKITI WA CCM RAIS DKT. SAMIA SULUHU HASSAN

Chimoio, Msumbiji — Agosti 22, 2026.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Wazazi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Comrade Ally Salum Hapi, amekutana na kufanya mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Msumbiji ambaye pia ni Rais wa Chama cha FRELIMO, Mhe. Daniel Francisco Chapo.

Mazungumzo hayo yamefanyika jijini Chimoio, Msumbiji, wakati Comrade Hapi akimwakilisha Katibu Mkuu wa CCM, Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro, katika Kongamano la 11 la Kitaifa la Makada wa FRELIMO linaloongozwa na Rais Daniel Chapo.

Kongamano hilo ni sehemu ya maandalizi kuelekea Mkutano Mkuu wa Chama cha FRELIMO unaotarajiwa kufanyika mwaka 2027.

Katika mazungumzo hayo, Comrade Hapi amewasilisha salamu za kheri, udugu na ushirikiano kutoka kwa Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa Rais Chapo na chama cha FRELIMO.

Hapi amesema uhusiano kati ya CCM na FRELIMO ni wa kihistoria na wa kindugu, uliyojengwa tangu enzi za harakati za ukombozi wa Afrika, na umeendelea kuimarika katika nyanja mbalimbali.

Chama cha FRELIMO kilianzishwa jijini Dar es Salaam, Tanzania, tarehe 25 Juni 1962, wakati Tanzania ikiwa kitovu muhimu cha harakati za ukombozi wa mataifa ya Kusini mwa Afrika.

Uhusiano huo wa kihistoria umeendelea kuwa msingi muhimu wa ushirikiano kati ya Tanzania na Msumbiji, pamoja na vyama vya CCM na FRELIMO, katika kuendeleza mshikamano, amani na maendeleo ya wananchi wa nchi hizo mbili.

Mazungumzo ya Hapi na Rais Chapo yanaongeza msukumo katika kuendeleza uhusiano wa karibu kati ya vyama hivyo viwili vya ukombozi na kuimarisha ushirikiano wao kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.





Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, amefanya ziara ya kushtukiza katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mwananyamala, jijini Dar es Salaam, kwa lengo la kukagua hali ya utoaji wa huduma kwa wananchi.

Waziri Mkuu amefanya ziara hiyo leo Jumapili, Agosti 23, 2026, ambapo baada ya kuwasili hospitalini hapo ametembelea wodi mbalimbali, zikiwemo Wodi ya Mama na Mtoto pamoja na Wodi ya Upasuaji.

Akiwa katika wodi hizo, Dkt. Nchemba amezungumza na wagonjwa pamoja na ndugu zao, kusikiliza maoni yao kuhusu huduma wanazopata na kufahamu changamoto zinazowakabili wakati wa kupata matibabu.

Wananchi waliokutana na Waziri Mkuu wamempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na Serikali kwa juhudi zinazoendelea katika kuboresha huduma za afya na mazingira ya utoaji wa huduma hospitalini.

Ziara hiyo imefanyika ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali za kufuatilia kwa karibu utoaji wa huduma za kijamii na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora, kwa wakati na katika mazingira yanayokidhi mahitaji yao.

Katika ziara hiyo, Waziri Mkuu ameambatana na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila; Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Mhe. Saad Mtambule; pamoja na viongozi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mwananyamala.








Top News