Na Janeth Raphael - MichuziTv


Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) imeweka mikakati ya muda mrefu ya kuimarisha ubora wa elimu, utafiti, ubunifu, matumizi ya TEHAMA na miundombinu, ikiwa sehemu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050 na mipango ya Serikali ya kuendeleza rasilimali watu na taasisi za elimu nchini.

Afisa Mtendaji Mkuu wa TIA, Prof. William Amos Pallangyo, amesema hayo Septemba 7, 2026, jijini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari katika Ukumbi wa Idara ya Habari – MAELEZO kuhusu utekelezaji wa shughuli za taasisi hiyo katika mwaka wa fedha 2025/26 pamoja na mwelekeo wa mwaka wa fedha 2026/27 na miaka inayofuata.

Amesema mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha mwaka wa fedha 2025/26 yameweka msingi wa TIA kuchukua hatua zaidi katika kuboresha huduma za elimu na kuongeza uwezo wa taasisi hiyo kutoa wataalamu wenye ujuzi unaokidhi mahitaji ya Taifa.

Prof. Pallangyo amesema katika mwaka wa fedha 2026/27 na miaka inayofuata, TIA itaendelea kutekeleza mipango yake kwa kuzingatia Dira ya Taifa 2050, Mpango Mkakati mpya wa TIA wa mwaka 2026/27–2030/31 pamoja na miongozo ya Serikali.

Amesema moja ya vipaumbele vya taasisi hiyo ni kuongeza ubora wa elimu kwa kuimarisha uwezo wa wahadhiri na watumishi zaidi ya 400, sambamba na kuboresha mazingira ya kujifunzia, utafiti na utoaji wa ushauri wa kitaalamu. TIA pia inalenga kuboresha maktaba na huduma za intaneti ili kuwawezesha wanafunzi na watafiti kupata nyenzo muhimu za kitaaluma kwa urahisi zaidi.

Katika hatua nyingine, taasisi hiyo inalenga kuongeza matumizi ya TEHAMA katika utoaji wa huduma kwa wanafunzi pamoja na usimamizi wa shughuli za taasisi, hatua inayotarajiwa kuongeza ufanisi na kuboresha huduma kwa wadau wake.

Kwa upande wa miundombinu, Prof. Pallangyo amesema TIA inalenga kukamilisha miradi ya kimkakati katika Kampasi za Kigoma, Mwanza, Zanzibar na Singida ili kuongeza uwezo wa taasisi hiyo kutoa huduma bora za elimu katika maeneo hayo.

Amesema TIA pia inapanga kujenga jengo jipya la taaluma katika eneo la Gezaulole, Kigamboni, kwa ajili ya kuongeza uwezo wa Kampasi ya Dar es Salaam na kupunguza msongamano uliopo katika Makao Makuu ya taasisi hiyo.

Aidha, TIA inalenga kupata eneo kwa ajili ya ujenzi wa Kampasi mpya ya Tanga, huku ikiendelea na taratibu za kukamilisha suala la fidia ya eneo lililotengwa kwa ajili ya Kampasi ya Zanzibar.

Prof. Pallangyo amesema TIA pia inaandaa mpango wa miaka 25 wa mwaka 2026 hadi 2050, ambao utaweka mwelekeo wa muda mrefu wa taasisi hiyo katika maeneo mbalimbali ya kimkakati, yakiwemo elimu, utafiti, ubunifu, TEHAMA, miundombinu na ushirikiano wa kimataifa.

Amesema mpango huo utaendana na Dira ya Taifa 2050 pamoja na Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2025–2030, kwa lengo la kuhakikisha TIA inaendelea kujenga uwezo wa kitaaluma na kuzalisha wataalamu watakaokuwa na mchango katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii ya Tanzania.

“Mafanikio haya yanaweka msingi wa hatua nyingine kubwa zaidi,” amesema Prof. Pallangyo, akieleza kuwa TIA itaendelea kuchukua hatua za kimkakati katika kuimarisha elimu, utafiti na huduma zake ili kuendana na mahitaji ya Taifa katika safari ya kuelekea mwaka 2050.






Na Janeth Raphael - MichuziTv

Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kuimarisha Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) kwa kuongeza uwezo wa kitaaluma na kuboresha miundombinu yake, hatua inayolenga kuifanya taasisi hiyo kuwa na uwezo mkubwa zaidi katika kutoa elimu, kufanya tafiti, ubunifu na uzalishaji wa maarifa.

Katika kuimarisha rasilimali watu, Serikali imeiwezesha TIA kupata Maprofesa tisa pamoja na kufadhili watumishi 78 kusoma Shahada ya Uzamivu (PhD) ndani na nje ya nchi. Kati ya watumishi hao, 48 tayari wamehitimu masomo yao, huku 30 wakiendelea na masomo.

Afisa Mtendaji Mkuu wa TIA, Prof. William Amos Pallangyo, amesema hatua hiyo imeongeza idadi ya wataalamu wenye sifa za juu za kitaaluma na kuimarisha uwezo wa taasisi hiyo katika ufundishaji, utafiti, ubunifu na uzalishaji wa maarifa.

Amesema ongezeko hilo la uwezo wa kitaaluma limekwenda sambamba na upanuzi wa fursa za elimu ya juu, ambapo TIA imeweza kuanzisha programu za Shahada ya Uzamili katika kampasi zake za Zanzibar, Mbeya, Singida na Mwanza, hatua inayowezesha wananchi kutoka maeneo mbalimbali nchini kupata fursa zaidi za elimu ya juu.

Prof. Pallangyo amesema mafanikio hayo yamechochewa pia na uwekezaji mkubwa wa Serikali katika miundombinu ya elimu, ambapo katika kipindi cha miaka mitano jumla ya Shilingi bilioni 67.9 zimewekezwa katika ujenzi na uboreshaji wa miundombinu katika kampasi za TIA zilizopo Mtwara, Mbeya, Singida, Kigoma, Mwanza na Zanzibar.

Kati ya fedha hizo, Shilingi bilioni 27.8 zimetolewa kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET) chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. Fedha hizo zimetumika katika maeneo mbalimbali ikiwemo ujenzi wa miundombinu, TEHAMA, samani, mafunzo ya wahadhiri, maboresho ya mitaala, tathmini na shughuli nyingine za mradi.

Katika fedha hizo za HEET, Shilingi bilioni 22.6 zimeelekezwa moja kwa moja katika ujenzi wa miundombinu ya kampasi za Singida na Mwanza. Kwa upande wa Singida, ujenzi wa jengo la taaluma umefikia asilimia 72 na unatarajiwa kukamilika Septemba 28, 2026. Mradi huo wenye thamani ya Shilingi bilioni 14.7 unatarajiwa kuongeza uwezo wa kampasi hiyo kuhudumia wanafunzi hadi 3,650 na tayari umezalisha ajira 275.

Amesema katika Kampasi ya Mwanza, ujenzi wa mabweni kupitia mradi wa HEET umefikia asilimia 96. Mabweni hayo yatakapokamilika yataweza kuhudumia wanafunzi 306, wakiwemo wanawake 203 na wanaume 103, huku mradi huo ukiwa umegharimu Shilingi bilioni 7.9 na kuzalisha ajira 323.

Mbali na uwekezaji kupitia HEET, Serikali kupitia Wizara ya Fedha imewekeza Shilingi bilioni 45.2 katika miradi mbalimbali ya TIA katika kampasi za Mwanza, Kigoma, Zanzibar, Mbeya na Mtwara.

Katika Kampasi ya Mwanza, jengo la taaluma na utawala limekamilika na linaendelea kutumika, likiwa na uwezo wa kuhudumia wanafunzi 1,620 kwa wakati mmoja. Ujenzi wa jengo hilo umegharimu Shilingi bilioni 8.4 na umezalisha ajira 223.

Kampasi ya Kigoma nayo imepiga hatua ambapo jengo la taaluma na utawala limefikia asilimia 98 na tayari linatumika. Mradi huo wenye thamani ya Shilingi bilioni 11.5 umezalisha ajira 217.

Kwa upande wa Zanzibar, ujenzi wa jengo la taaluma, utawala na mabweni umefikia asilimia 45 na unaendelea. Mradi huo wenye thamani ya Shilingi bilioni 16.3 umezalisha ajira 130 hadi sasa na utakapokamilika utawezesha TIA kudahili wanafunzi 580 na kutoa huduma ya mabweni kwa wanafunzi 480.

Katika Kampasi ya Mbeya, ujenzi wa jengo lenye kumbi za mihadhara, maktaba na maabara ya kompyuta umekamilika kwa asilimia 100 na tayari linatumika. Jengo hilo lina uwezo wa kuhudumia wanafunzi 250 katika kumbi za mihadhara, wanafunzi 180 katika maktaba na wanafunzi 168 katika maabara ya kompyuta. Mradi huo umegharimu Shilingi bilioni 3.4 na umezalisha ajira 110.

Kwa upande wa Mtwara, Serikali imekamilisha ujenzi wa jengo la taaluma, maktaba, maabara ya kompyuta, mabweni pamoja na nyumba za watumishi. Mradi huo umegharimu Shilingi bilioni 5.6 na umezalisha ajira 334 wakati wa utekelezaji wake.

Miundombinu hiyo ina uwezo wa kuhudumia wanafunzi 175 katika maabara ya kompyuta, 200 katika maktaba na wanafunzi 650 katika madarasa manne. Aidha, mabweni yana uwezo wa kuchukua wanafunzi 324, wakiwemo wanaume 212 na wanawake 112.

Prof. Pallangyo amesema uwekezaji huo mkubwa wa Serikali haujalenga kuboresha majengo ya TIA pekee, bali umeongeza uwezo wa taasisi hiyo kuhudumia wanafunzi wengi zaidi, kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia pamoja na kuimarisha shughuli za kitaaluma na uzalishaji wa maarifa.

Amesema pia uwekezaji huo umeleta manufaa kwa jamii zinazozunguka kampasi hizo kwa kuchochea shughuli za kiuchumi, ikiwemo kuibua fursa za ajira na biashara ndogo ndogo kwa wananchi.

Prof. Pallangyo ameyasema hayo jijini Dodoma, Septemba 7, 2026, wakati akizungumza na waandishi wa habari katika Ukumbi wa Idara ya Habari – MAELEZO kuhusu utekelezaji wa TIA katika mwaka wa fedha 2025/26 pamoja na mwelekeo wa taasisi hiyo katika mwaka wa fedha 2026/27.




Serikali imesisitiza dhamira yake ya kuwalinda wawekezaji wa ndani katika sekta ya madini na kuhakikisha wanapata thamani zaidi kutokana na uwekezaji wao, wakati juhudi za kuongeza ushiriki wa Watanzania katika mnyororo mzima wa thamani wa sekta ya madini zikiendelea kushika kasi.

Dhamira hiyo ya serikali imesisitizwa na Kamishna wa Tume ya Madini ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini (Local Content), Dkt. Theresia Charles Numbi, wakati wa ziara yake kwenye kampuni ya Max Steel Limited, kampuni ya Kitanzania inayojihusisha na uhandisi na utengenezaji wa miundombinu kwa kutumia chuma kizito, ikiwemo miundo ya chuma, matanki, maghala makubwa ya kuhifadhia bidhaa (silos), chutes na miundombinu mingine maalumu kwa ajili ya miradi ya madini, ujenzi na viwanda.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Dkt. Numbi, alisema kuimarisha uwezo wa kampuni za ndani ni jambo muhimu katika kuongeza ushiriki wa Watanzania kwenye mnyororo wa thamani wa madini na kuhakikisha taifa linapata manufaa makubwa zaidi ya kiuchumi kutokana na rasilimali zake za madini.

Ziara hiyo ilifanyika muda mfupi baada ya Jukwaa la Uzingatiaji wa Matakwa ya Maudhui ya Ndani (Local Content Compliance Forum), lililowakutanisha viongozi wa Serikali, kampuni za madini, wakandarasi, wasambazaji, wazalishaji na wadau wengine kujadili utekelezaji wa matakwa ya maudhui ya ndani.

Jukwaa hilo pia lilisisitiza umuhimu wa kuhakikisha kuwa sera, ahadi na mijadala ya wadau vinatafsiriwa kuwa ongezeko la ushiriki wa Watanzania, uwekezaji na uwezo wa uzalishaji wa viwanda nchini.

Katika ziara hiyo, Dkt. Numbi alisema Serikali imebaini pengo ambalo linaweza kusababisha wachimbaji wadogo na wa kati kubaki nyuma wakati sekta ya madini nchini ikiendelea kukua.

Aliwataka wawekezaji na wazalishaji waliokwisha jenga uwezo mkubwa katika sekta hiyo kusaidia kukuza shughuli za waendeshaji wadogo kwa kuwawezesha kupata teknolojia zinazowafaa, utaalamu wa kitaalamu, mafunzo ya ujuzi pamoja na vifaa na miundombinu inayozalishwa nchini.

“Serikali inataka kuona wawekezaji wa ndani wakipata thamani kutokana na rasilimali na fursa zilizopo katika sekta ya madini. Wakati huo huo, ukuaji wa kampuni zilizoimarika unapaswa kuleta fursa kwa wachimbaji wadogo na wa kati kushiriki kwa maana zaidi katika sekta hii,” alisema.

Wakati wa ziara hiyo, Afisa Mkuu wa Uendeshaji wa Max Steel, Bi. Bhavna Pandya, alimweleza Dkt. Numbi kuhusu shughuli za kampuni hiyo, uwekezaji uliofanyika pamoja na mipango yake ya upanuzi.

Dkt. Numbi aliipongeza Max Steel kwa uwekezaji wake katika uzalishaji wa ndani na kwa kutengeneza ajira kwa zaidi ya Watanzania 140.

Alisema ajira na mafunzo ya kitaalamu yanayotolewa na kampuni hiyo yanaendana na vipaumbele vya Serikali vya kuongeza ajira, kuendeleza viwanda na kuongeza ushiriki wa Watanzania katika sekta zinazohitaji utaalamu maalumu.

Alivutiwa zaidi na uwekezaji wa kampuni hiyo katika maendeleo ya ujuzi na uhamishaji wa teknolojia, akibainisha kuwa shughuli za Max Steel zinawapa wahandisi, mafundi, wachomeleaji, wataalamu wa uundaji wa miundombinu ya chuma, wasimamizi na menejimenti wa Kitanzania uzoefu wa vitendo katika uhandisi wa chuma kizito na utekelezaji wa miradi mikubwa na changamano ya madini na viwanda.

“Kujenga maudhui ya ndani kunamaanisha kuwaendeleza watu kwa kiwango sawa na tunavyojenga viwanda. Maarifa na uwezo wa kitaalamu unaotokana na uwekezaji huu vinapaswa kubaki Tanzania na kuendelea kuimarisha msingi wa viwanda nchini,” alisema Dkt. Numbi.

Aidha, Dkt. Numbi alisema ushirikiano wa karibu kati ya Serikali, kampuni za madini na wazalishaji wa ndani utakuwa muhimu katika kukabiliana na changamoto zinazowakabili wachimbaji wadogo na wa kati.

Alihimiza kampuni zilizoimarika kuanzisha ushirikiano wa vitendo utakaowawezesha waendeshaji wadogo kupata utaalamu wa kitaalamu, teknolojia zinazowafaa na suluhisho za kuaminika zinazozalishwa hapa nchini.

Akizungumza katika hafla hiyo, Bi. Pandya, alisema thamani ya muda mrefu ya maudhui ya ndani haipaswi kupimwa kwa kuangalia tu kiwango cha bidhaa na huduma zinazonunuliwa ndani ya nchi, bali pia kwa kuangalia uwezo wa uzalishaji, maarifa ya kitaalamu na ajira zinazozalishwa ndani ya Tanzania.

“Maudhui ya ndani hayawezi kumaanisha kununua bidhaa hapa nchini pekee. Yanapaswa kumaanisha kujenga uwezo wa kutengeneza, kujenga na kutoa huduma hapa nchini. Kama Tanzania inaweza kutengeneza tanki la CIL, kutengeneza chute au silo hapa nchini, kuwaajiri Watanzania kufanya kazi hizo na kuendeleza ujuzi wa kuzifanya vizuri zaidi wakati ujao, huo ndio uzalishaji wa ndani unaojenga uwezo wa viwanda wa kudumu,” alisema.

Kwa sasa, Max Steel ina uwezo wa kutengeneza takribani tani 800 kwa mwezi. Kampuni hiyo inaendelea na mpango wa upanuzi unaotarajiwa kuongeza uwezo wake hadi takribani tani 1,200 kwa mwezi, hatua itakayoipa uwezo wa kutekeleza miradi mikubwa zaidi na yenye mahitaji ya juu ya kitaalamu.

Pandya aliipongeza Serikali kwa kuendelea kusisitiza utekelezaji wa maudhui ya ndani, lakini akaiomba kuweka sera zitakazowawezesha wazalishaji wa Kitanzania kushindana kwa usawa na wasambazaji wa bidhaa zilizokamilishwa kutoka nje ya nchi.

Alisisitiza haja ya kupitia upya ushuru wa forodha na kodi zinazotozwa kwenye malighafi za viwandani zinazotumiwa na wazalishaji wa ndani, akieleza kuwa gharama hizo zinaweza kufanya bidhaa zinazozalishwa nchini kuwa ghali zaidi kuliko bidhaa zilizokamilishwa zinazoagizwa kutoka nje.

“Pale malighafi zinapotozwa ushuru unaofanya bidhaa zinazozalishwa nchini kuwa ghali kuliko bidhaa zilizokamilishwa zinazoagizwa kutoka nje, viwanda vya ndani huanza mashindano vikiwa tayari nyuma. Hatuombi kulindwa dhidi ya ushindani. Tunachoomba ni mazingira ya haki ya kufanya biashara yanayotambua ajira, ujuzi, kodi na uwezo wa uzalishaji unaojengwa pale bidhaa zinapotengenezwa Tanzania,” alisema Pandya.

Alisema msaada wa kifedha unaolenga malighafi za viwandani na vifaa vya uzalishaji ungewezesha kampuni za ndani kupanua shughuli zao, kuongeza ajira na kushindana kwa ufanisi kwa kuzingatia ubora, uaminifu wa bidhaa na huduma pamoja na bei.

Ziara hiyo imeonesha uwezo unaokua wa Max Steel katika kusaidia utekelezaji wa miradi mikubwa ya madini na viwanda, huku wakati huo huo ikitoa ajira, kuwezesha uhamishaji wa teknolojia na kuimarisha mnyororo wa ugavi wa ndani nchini Tanzania.

Kupitia mpango wake wa upanuzi na uwekezaji unaoendelea katika wataalamu wa Kitanzania, Max Steel inalenga kuongeza kiwango cha miundombinu inayohitajika na sekta ya madini kinachoweza kutengenezwa ndani ya nchi, huku ikisaidia kuhakikisha sehemu kubwa zaidi ya thamani ya kiuchumi inayotokana na shughuli hizo inabaki nchini Tanzania.

Kamishna wa Tume ya Madini ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini (Local Content), Dkt. Theresia Charles Numbi (wa tatu kutoka kushoto), akiwa katika picha ya pamoja na Afisa Mkuu wa Uendeshaji wa Max Steel, Bi. Bhavna Pandya (wa nne kutoka kushoto), pamoja na wafanyakazi wa kampuni hiyo, wakati wa ziara yake katika kampuni hiyo jijini Dar es Salaam hivi karibuni.

Kamishna wa Tume ya Madini ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini (Local Content), Dkt. Theresia Charles Numbi (katikati), akisikiliza taarifa kuhusu uendeshwaji wa shughuli za kampuni ya Max Steel kwa Afisa Mkuu wa Uendeshaji wa kampuni hiyo Bi. Bhavna Pandya (wa pili kulia), wakati wa ziara yake katika kampuni hiyo jijini Dar es Salaam hivi karibuni.

Baadhi ya wafanyakazi wa kampuni ya Max Steel wakiendelea na majukumu yao.

Afisa Mkuu wa Uendeshaji wa kampuni ya Max Steel Bi. Bhavna Pandya (wa sita kulia – mbele) akiwa kwenye picha ya pamoja na wafanyakazi wa kampuni hiyo wakati wa ziara hiyo.

Kamati ya kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji kwa Umma mwishoni mwa wiki iliyopita imetembelea eneo la hifadhi ya Ngorongoro ambapo pamoja na mambo mengine imejionea vivutio vya utalii ikiwemo mchanga unaohama ambao haupatikani popote Duniani isipokuwa Ngorongoro.

Wakiongozwa na Mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Masanja Kadogosa, wabunge hao wameshauri Ngorongoro na wadau wa utalii kuongeza nguvu katika kuvitangaza vivutio tulivyonavyo kimataifa hasa mchanga huo, bonde la Olduvai, kazi zilizofanywa na watafiti mbalimbali kama Dkt. Luis na Mary Leakey, historia ya binadamu wa kale na ugundunzi wa Nyayo za Laetoli miaka milioni 3.6 iliyopita

“Ukweli ni kwamba Ngorongoro mna mtaji mkubwa wa kuingiza fedha za kigeni na watalii wengi, ni hifadhi ya aina yake, tunachowashauri ni kuongeza nguvu ya kutangaza vivutio hivi katika anga za kimataifa”, alisema mhe Kadogosa kwa niaba ya kamati.

Makamu mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Mamlaka hiyo Dkt.Harriet Mtae ambaye pia ni Mhadhiri Mwandamizi kutoka Chuo Kikuu Huria cha Tanzania aliwashukuru wabunge hao kwa maelekezo mbalimbali yenye lengo la kuboresha utendaji kazi wa Hifadhi ya Ngorongoro na kuahidi kuyafanyia kazi.

Naibu Kamishna wa Mamlaka hiyo anayesimamia huduma za shirika Aidan Makalla aliwaeleza wabunge hao kuwa Mamlaka imedhamiria kuboresha utoaji wa huduma na sasa imeanza ujenzi wa barabara kipande cha kwanza kutoka Loduare mpaka Seneto kuelekea Golini.






Katibu wa NEC – Uchumi na Fedha wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Jamal Kassim Ali, leo tarehe 6 Septemba 2026 amezindua rasmi mradi wa vibanda vya biashara kwa wajasiriamali wadogo unaomilikiwa na CCM Mkoa wa Kagera, mjini Bukoba.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa mradi huo, Ndugu Jamal ameipongeza CCM Mkoa wa Kagera kwa kutumia rasilimali za Chama kuanzisha mradi wenye tija, unaolenga kuchochea shughuli za kiuchumi, kuwawezesha wajasiriamali wadogo na kuongeza uwezo wa Chama katika kujitegemea.

Amesema wajasiriamali wadogo wa leo ndio msingi wa wawekezaji wakubwa wa kesho, hivyo amewataka viongozi, hususan madiwani, kutambua na kutumia fursa za kiuchumi zilizopo katika kata zao ili kuwawezesha vijana kujiajiri na kujenga uchumi wa maeneo yao.

Aidha, Ndugu Jamal amewataka wanachama wa CCM kuishi kwa vitendo Imani na misingi ya Chama, akisisitiza umuhimu wa nidhamu, usawa na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu ya Chama.

Amesema hakuna mwanachama aliye juu ya Chama, na kwamba kila mwanachama anapaswa kuheshimu Katiba, kanuni na taratibu za CCM bila kujali nafasi au cheo alichonacho.

“Hakuna mtu aliye juu ya CCM; wanachama wote ni sawa mbele ya Katiba, kanuni na taratibu za Chama.”







▪️︎ Atoa rai kwa Watanzania kuchukua tahadhari dhidi ya mafuriko

▪️︎ Aagiza ndani ya Septemba kutangazwa zabuni ya ujenzi wa barabara km 11 za Igauri–Ilongero

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, ametoa wito kwa Watanzania na viongozi katika ngazi zote kuchukua tahadhari na kujiandaa mapema kukabiliana na athari zinazoweza kujitokeza kutokana na mvua kubwa zinazohusishwa na hali ya El Niño.

Dkt. Mwigulu ametoa rai hiyo leo, Jumapili, Septemba 06, 2026, wakati akizungumza na wananchi wa Jimbo la Ilongero, Wilaya ya Singida, mkoani Singida, katika ziara yake ya kikazi ya kusikiliza kero za wananchi na kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Amesema maeneo yenye historia ya mafuriko yanapaswa kutambuliwa mapema na hatua za tahadhari kuchukuliwa, huku akiwataka wananchi wanaoishi katika maeneo hatarishi kuzingatia taarifa na maelekezo ya mamlaka husika.

“Maeneo ambayo mnaona ni ya hatari sana Watanzania tunayajua. Tunayajua maeneo yenye historia ya mafuriko. Ni vyema tukaanza kuchukua tahadhari kwa sababu hicho ndicho tunachoweza kukifanya,” alisema.

Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea kuimarisha uwezo wa kukabiliana na athari za mvua, ikiwemo kuwa na magari ya kuchimba mabwawa katika kila ukanda, huku akisisitiza kuwa wananchi wanapaswa kuepuka kujenga au kuishi katika maeneo yanayofahamika kuwa hatarishi kwa mafuriko.

Kuhusu barabara ya Igauri–Ilongero, Dkt. Mwigulu ametoa agizo la kuhakikisha ndani ya mwezi huu mchakato wa kumpata mkandarasi wa ujenzi wa kilomita 11 za awali unakamilika.

“Ndani ya mwezi huu huu, muwe mmeshatangaza kupata mkandarasi wa kuanza kujenga hizi kilomita 11 za awali ambazo zitaziba hili pengo kuanzia hapa mpaka kwenye lami na kupita kidogo mji wa Ilongero,” alisema.

Alisema fedha kwa ajili ya mradi huo zipo na kinachosubiriwa ni kumpata mkandarasi, akisisitiza kuwa ujenzi huo unapaswa kuanza haraka.

Dkt. Mwigulu pia amesisitiza umuhimu wa Serikali kubana matumizi yasiyo ya lazima na kuelekeza fedha zinazookolewa kwenye maeneo yenye kipaumbele, hususan elimu, afya, maji na miundombinu.

Amesema hatua hiyo ni muhimu kutokana na ongezeko kubwa la wanafunzi wanaotarajiwa kuingia kidato cha kwanza kuanzia mwaka 2028, hivyo Serikali inapaswa kuanza mapema maandalizi ya madarasa, maabara, maktaba na mahitaji mengine ya elimu.

“Ni fedha ya Serikali, ni fedha ya walipa kodi wa Tanzania, ni fedha ambayo inaweza kwenda kutatua hizi changamoto watoto wasikae chini,” alisema.

Kuhusu afya, Waziri Mkuu amesisitiza kuwa ambulensi zinapaswa kuwa tayari muda wote na kuwa na mafuta ili wagonjwa wanaohitaji huduma za dharura na rufaa wasicheleweshwe.

“Ambulensi zetu ziwe standby. Tulishanunua magari, yawe na mafuta. Kila wakati yawe na mafuta. Tusichangishe wagonjwa kuweka mafuta kwenye gari ya Serikali kubeba mgonjwa ambaye yuko mautini,” alisema.

Aidha, ametoa wito kwa Watanzania kujiunga na Bima ya Afya kwa Wote, akisema mfumo huo ni suluhisho la kudumu la kupunguza utegemezi wa michango ya dharura wakati wananchi wanapokabiliwa na gharama za matibabu.

“Watanzania wote tuingie kwenye bima ya afya. Tutaepukana na matatizo mengi sana ambayo tumeyatafutia majawabu ya dharura, lakini yanahitaji yapate majawabu ya kudumu,” alisema.

Kuhusu maji, Dkt. Mwigulu amesema Serikali itaendelea kutekeleza miradi ya maji na umwagiliaji kwa ushirikiano wa wizara zinazohusika, ili miradi hiyo iweze kunufaisha wananchi, mifugo na shughuli za uzalishaji.

Amesema Serikali itaendelea kusimamia matumizi yenye tija ya rasilimali za umma na kuhakikisha miradi ya maendeleo inatekelezwa kwa kuzingatia thamani ya fedha, ufanisi na mahitaji halisi ya wananchi.











Na, Mwandishi Wetu -Dodoma

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuzindua majengo ya Ofisi za Wizara, Taasisi za Serikali pamoja na barabara za lami zenye urefu wa kilomita 57.1 katika Mji wa Serikali Mtumba,Jijini Dodoma.

Uzinduzi huo unatarajiwa kufanyika jumanne Septemba nane mwaka huu katika Uwanja wa Mashujaa uliopo ndani ya Mji wa Serikali Mtumba.

Hayo yamebainishwa Jijini Dodoma leo (06 Septemba, 2026) na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Mhe.Profesa Palamagamba Kabudi, wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maandalizi ya hafla hiyo.

Alisema uzinduzi huo utahusisha maeneo matatu makuu ambayo ni majengo ya Ofisi za Wizara 26, Taasisi 11 za Serikali na barabara za lami zenye urefu wa kilomita 57.1.

Profesa Kabudi alisema kukamilika kwa majengo hayo, kutawezesha watumishi 18,510 kutumia ofisi za Mji wa Serikali, Mtumba.

“Ujenzi wa Mji wa Serikali Mtumba ulianza kutekelezwa kwa awamu, ambapo awamu ya kwanza ilihusisha ujenzi wa majengo 23 ya Ofisi za muda.ujenzi wa majengo hayo ulianza Novemba 28 mwaka 2018 na kukamilika Machi 22 mwaka 2019, hatua iliyowezesha baadhi ya watumishi wa Wizara na taasisi kuanza kuhamia.

Aliongeza kuwa :” Awamu ya pili ya ujenzi ilianza Oktoba, 2021, ikiwa inalenga kujenga majengo ya kudumu kwa ajili ya watumishi wote wa Wizara na Taasisi zilizopangwa kuhamia Mtumba.Pia ilihusisha ujenzi wa miundombinu na huduma mbalimbali za kijamii, ikiwemo barabara za lami.

Profesa Kabudi alisema mbali na barabara hizo, miundombinu ya kudumu ya mawasiliano pamoja na Uwanja wa Mashujaa imekamilika na itakuwa sehemu ya miundombinu itakayotumika katika shughuli za Serikali.

Hata hivyo, alisema baadhi ya miradi bado iko katika hatua mbalimbali za utekelezaji, ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya umeme inayopita chini ya ardhi yenye urefu wa kilomita 42.

“Kazi ya ujenzi wa miundombinu ya maji safi na uondoshaji wa maji taka, TEHAMA, ufungaji wa mifumo ya usalama ya CCTV Camera, ujenzi wa kituo cha zimamoto pamoja na utekelezaji wa mpango wa upandaji miti na ustawishaji wa Mji wa Serikali nazo zinafanyika, "alisema.

Alisema Rais Dkt.Samia ameendelea kuweka msisitizo katika kuboresha mazingira hayo, ikiwa ni pamoja na kutoa fedha kwa ajili ya ununuzi wa samani za Wizara na taasisi 26 zinazohamia katika majengo hayo.

Profesa Kabudi alisema hatua hizo zinaendelea kuifanya Mji wa Serikali Mtumba kuwa miongoni mwa alama muhimu za utekelezaji wa dhana ya Dodoma kuwa kitovu cha shughuli za Serikali.

Alisema uwekezaji huo pia unatarajiwa kuongeza fursa za kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa Dodoma na Tanzania kwa ujumla.






Benki ya Exim Tanzania inaadhimisha miaka 29 tangu kuanzishwa kwake chini ya kaulimbiu "Miaka 29 ya Ubora kwa Vitendo," ikisherehekea karibu miongo mitatu ya ukuaji, uhusiano na wateja, ushirikiano na mchango kwa jamii inazozihudumia.

Mwaka 1997, Benki ya Exim Tanzania ilianza safari yake ikiwa na idadi ndogo ya wateja, na hatua kwa hatua ikajenga uwepo wake katika soko la Tanzania. Kwa kipindi cha miaka 29, Benki imekua na kuwa mojawapo ya taasisi za kifedha zinazoongoza nchini Tanzania, ikitambulika kwa ubunifu wake, suluhisho zinazomlenga mteja na mchango wake mkubwa katika ukuaji wa kiuchumi wa nchi, ikiwa na zaidi ya matawi 30 nchini kote na uwepo nje ya Tanzania katika masoko ya Comoro, Djibouti, Uganda na Ethiopia.

Kama sehemu ya safari hii, Benki ya Exim ilikuwa benki ya kwanza ya Tanzania kufungua matawi nje ya nchi, na kuifanya kuwa mojawapo ya benki chache za Tanzania zilizofanikiwa kupanua shughuli zake nje ya mipaka ya taifa hili. Kupitia mtandao wake mpana wa matawi na mifumo ya kisasa ya kibenki ya kidijitali, Benki inaendelea kuwawezesha watu binafsi na wafanyabiashara kwa suluhisho za kifedha zenye kutegemewa, nyumbufu na zinazolenga mustakabali, ikithibitisha dhamira yake ya kuchochea ukuaji endelevu na ustawi katika ukanda huu.

Safari ya Benki hii, hata hivyo, imekwenda mbali zaidi ya kutoa huduma za kifedha. Kwa miaka mingi, Benki ya Exim imewekeza katika mipango inayochangia ustawi na maendeleo ya jamii kupitia jukwaa lake la Exim Cares, likiwa na programu zinazogusa afya, elimu, ustawi wa vijana, uwezeshaji wa wanawake na uhifadhi wa mazingira. Mipango hii ni pamoja na msaada wa muda mrefu kwa kampeni za uchangiaji damu, ushirikiano na Young Scientists Tanzania (YST), Women Empowerment Program, pamoja na afua mbalimbali za kusaidia taasisi za afya na uhifadhi wa mazingira.

Mwaka huu, Benki inafanya maadhimisho yake kwa namna tofauti kwa kuupeleka mkondo huo moja kwa moja kwa jamii inazozihudumia. Kama sehemu ya maadhimisho ya miaka 29, Benki ya Exim imekuwa ikifanya shughuli za usafi wa mazingira na kukabidhi vifaa vya usafi katika maeneo mbalimbali kupitia mtandao wake wa matawi, ikiwemo masoko, hospitali na shule katika mikoa mbalimbali, kwa lengo la kuhakikisha kunakuwa na mazingira safi, salama na yenye afya kwa jamii.

Jijini Dar es Salaam, shughuli hizo ni pamoja na ukabidhi wa vifaa vya usafi kwa Manispaa ya Kinondoni na zoezi la usafi wa jamii katika Fukwe ya Kawe, likikutanisha wafanyakazi wa Benki ya Exim, wadau na wanajamii katika kuchangia maeneo safi na yenye afya zaidi.

Akizungumza wakati wa maadhimisho hayo, Mkuu wa Idara ya Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania, Bw. Stanley Kafu, alisema maadhimisho ya miaka 29 yanatoa fursa ya kuwathamini watu na jamii ambazo zimekuwa muhimu katika safari ya Benki, huku ikithibitisha dhamira yake ya kuendelea kuleta thamani zaidi siku zijazo.

"Safari yetu ya miaka 29 imejengwa pamoja na wateja wetu, wafanyakazi, washirika na jamii tunazozihudumia. Kila mteja aliyetuamini, kila biashara tuliyoisaidia na kila ushirikiano tulioujenga umechangia kuifanya Benki ya Exim kuwa taasisi iliyopo leo. Maadhimisho haya kwa hiyo si tu kuhusu kusherehekea Benki ya Exim; ni kuhusu kusherehekea kila mmoja aliyekuwa sehemu ya safari yetu," alisema Bw. Kafu.

Aliongeza kuwa uamuzi wa kuadhimisha maadhimisho hayo kupitia shughuli za kijamii unaakisi imani ya Benki kwamba dhamira yake inakwenda mbali zaidi ya huduma za kifedha.

"Tunafanya maadhimisho kwa namna tofauti mwaka huu kwa kuubadilisha mkondo huu kuwa kitu chenye maana kwa jamii zinazotuzunguka. Usafi wa mazingira ni jukumu la pamoja, na kupitia shughuli hizi na ukabidhi wa vifaa vya usafi, tunachangia kwa vitendo huku tukihamasisha watu wengi zaidi kumiliki maeneo tunayoyashiriki sote. Hii ndiyo maana halisi ya Ubora kwa Vitendo, kubadilisha dhamira kuwa hatua za vitendo zenye thamani kwa jamii zinazotuzunguka," alisema.

Akizungumza kwa niaba ya jamii, Diwani wa Kata ya Kawe, Bw. Benard Fabian Malima, alipongeza Benki ya Exim kwa kuchagua Kawe kama mojawapo ya maeneo ya shughuli zake za maadhimisho.

"Kwa niaba ya wakazi wa Kawe, napenda kuishukuru Benki ya Exim kwa mpango huu. Fukwe ya Kawe ni eneo linalotumiwa na watu wengi katika jamii hii kila siku, na kuliweka safi ni jambo linalonufaisha sote. Ukabidhi wa vifaa vya usafi kwa Halmashauri yetu utasaidia sana jitihada zetu za kuendelea kuweka mazingira safi, na tunatarajia taasisi nyingine zaidi zitafuata mfano huu," alisema Bw. Malima.

Shughuli hizo za kijamii zilifanyika katika maeneo mbalimbali kupitia mtandao wa Benki ya Exim, zikiwawezesha wafanyakazi na wadau katika jamii mbalimbali kushiriki katika mpango huu wa maadhimisho.

Aidha, Benki ya Exim inapoelekea mwaka wake wa 30, inaendelea kuwa na dhamira ya kujenga juu ya safari yake ya miaka 29 kwa kuendelea kubuni, kuboresha uzoefu wa wateja, kusaidia biashara na kuleta thamani zaidi kwa wateja wake, wadau na jamii.
Mkuu wa Kitengo cha Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania Stanley Kafu (wa pili kulia) wakipeana mikono na Diwani wa Kata ya Kawe Mheshimiwa Fabian Malima (katikati) baada ya kukabidhi vifaa vya kufanyia usafi wa jiji. Shughuli hiyo imefanyika kama kilele cha kusherehekea miaka 29 ya Benki ya Exim toka uanzishwaji wake nchini ambapo, walishiriki pia katika usafi wa fukwe za bahari katika maeneo ya Kawe. Tukio hilo limefanyika  tarehe 5 Septemba 2026, jijini Dar es salaam na kushuhudiwa na Meneja Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania, Kauthar D'souza (kulia), Mkuu wa Kituo cha Polisi Kawe ASP Ally Liviga (kushoto) na Afisa Usafishaji Manispaa ya Kinondoni Alban Mugyabuso wa pili Kulia.





Uongozi wa Mamlaka ya Hifadhi ya eneo la Ngorongoro (NCAA) umeeleza kuwa, umedhamiria kuendelea kuboresha utoaji huduma kwa watalii kwa njia za kisasa kupitia matumizi ya teknolojia ya habari na mawasiliano ili kuongeza ufanisi na kasi ya utendaji kazi na ukusanyaji wa mapato.

Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa uhifadhi anayesimamia huduma za Utalii na Masoko Mariam Kobelo ameeleza kuwa lengo la kufanya kazi kidigitali ni kuhakikisha kuwa watoa huduma katika sekta ya utalii wanatumia muda mfupi kuingia na kutoka ndani ya hifadhi pamoja na kuhakikisha maduhuli ya serikali yanakusanywa kikamilifu na kuimarisha usalama wa hifadhi na rasilimali zilizopo.

“Siku mbili zilizopita tumekuwa na changamoto ndogo ndogo katika lango kuu la Ladoure ,tunaendelea kuzitatua kwa ushirikiano mkubwa na wadau wetu”,amesema bi.Kobelo.

Amewashukuru waongoza watalii wote na wadau katika sekta hiyo kwa kuonesha ushirikiano wa kutosha katika kufanikisha maboresho hayo.

Ameongeza kuwa mteja yeyote atakayekutana na changamoto za kiutendaji katika kipindi hiki ni vema akawasiliana na maafisa wa mamlaka hiyo ambao wapo katika lango hilo na maeneo mengine na watasaidiwa ili waweze kuendelea na safari zao kwa muda kama walivyopanga.

Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro katika mwelekeo wa utendaji wake mpya imedhamiria kuimarisha shughuli zake za kutoa huduma bora kwa watalii katika viwango vya kimataifa na kuendelea kuimarisha dawati la huduma na ukarimu kwa wateja.










Serikali imeutaka Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) kujipanga kikamilifu katika maandalizi ya mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027, hususan katika kuhakikisha wageni watakaofika nchini wanapata huduma bora za matibabu bila vikwazo.

Agizo hilo limetolewa l na Naibu Waziri wa Afya Mhe. Dkt. Florence Samizi (Mb.) ambaye amesema NHIF ina jukumu muhimu la kuratibu suala la bima ya afya wakati wa mashindano hayo ili kuhakikisha wageni wanapata huduma za matibabu kwa urahisi pindi wanapohitaji huduma hizo.

“Tuwape uhakika wa huduma bora ili waone fahari kuwapo hapa nchini katika kipindi chote cha mashindano hayo,” amesema Dkt. Samizi.

Amesema maandalizi ya huduma za matibabu yanapaswa kuzingatia pia huduma za dharura pamoja na huduma maalum, ikiwemo za moyo na mifupa, ili kukidhi mahitaji mbalimbali ya afya yatakayoweza kujitokeza wakati wa mashindano.

Aidha alidokeza kuwa tayari Wataalamu kutoka Shirikisho la Soka Afrika (CAF) wamekagua Vituo vya kutolea huduma kwa alengo la kujiridhisha na wamefurahishwa na utayari unaoonyeshwa katika maandalizi ya huduma za matibabu jambo linaloonesha kuwa Tanzania inajiandaa kuhakikisha AFCON 2027 inafanyika katika mazingira salama na yenye huduma bora.

Ameitaka NHIF kushirikiana kwa karibu na Wizara ya Afya, vituo vya kutolea huduma na wadau wengine kuhakikisha mfumo wa huduma za matibabu wakati wa mashindano hayo unakuwa imara, unaopatikana kwa wakati na unaokidhi viwango vinavyohitajika.

Akizungumzia hilo Mkurugenzi Mkuu waa NHIF, Dkt. Irene Isaka alisema kuwa tayari Mfuko umeshajipanga na umeandaa kifurushi maalumu kwa ajili ya wageni wote watakaokuja nchini kwa ajili ya mashindano hayo.

“Tayari tumejipanga na tuna kifurushi ambacho tutakileta Wizarani ili tupate baraka ya Wizara hivyo tunashukuru sana kwa maelekezo haya ambayo yanaboresha na kuhakikisha tunajipanga vyema,” alisema Dkt. Isaka. ‎


Top News