WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali chini ya uongozi wa Rais. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuweka mazingira wezeshi ya kukuza vipaji vya vijana kupitia uwekezaji katika sekta ya michezo na ujenzi wa miundombinu ya kisasa.

Akizungumza usiku wa kuamkia leo, Julai 31 2026 wakati tamasha la mchezo wa Masumbwi “Knockout ya Mama Season 9” liliofanyika katika ukumbi wa The super Dome Masaki jijini Dar es Salaam, Waziri Mkuu amesisitiza mpango wa Serikali kujenga arena kubwa ya kisasa itakayokuwa kitovu cha matukio mbalimbali ya michezo na burudani nchini.

Amesema Rais Samia Suluhu Hassan anaendelea kuunga mkono juhudi za vijana na wadau wa michezo nchini, huku Serikali ikiendelea kushirikiana kwa karibu na sekta binafsi katika kuimarisha maendeleo ya michezo na kuibua vipaji.



Na Farida Mangube
Mtanzania Bi. Rehema Katuga kutoka Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria nchini (OCPD) ameibuka mshindi katika uchaguzi wa wajumbe wa Baraza la Uongozi na Usimamizi la Chama cha Wataalamu wa Uandishi wa Sheria wa Jumuiya ya Madola (Commonwealth Association of Legislative Counsel – CALC), na kuwa mmoja wa wawakilishi wawili wa Afrika katika baraza hilo.

Baraza hilo, lenye wawakilishi wawili kutoka kila bara, lina jukumu la kusimamia na kufanya maamuzi muhimu kuhusu uendeshaji wa chama hicho cha kitaaluma kinachowakutanisha wataalamu wa uandishi wa sheria kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Madola.

Bi. Katuga aliibuka mshindi katika uchaguzi uliowahusisha wagombea wanne kutoka Afrika, wakiwemo wagombea wawili kutoka Afrika Kusini, mmoja kutoka Namibia na yeye akiwa mwakilishi pekee kutoka Tanzania. Ushindi huo umeiwezesha Tanzania kupata nafasi ya uwakilishi katika chombo hicho muhimu cha kitaaluma.

Akizungumzia umuhimu wa CALC, Bi. Katuga alisema chama hicho ni miongoni mwa vyama vya kitaaluma vinavyosimamiwa na Jumuiya ya Madola na kina jukumu la kuimarisha ushirikiano miongoni mwa wataalamu wa uandishi wa sheria katika nchi wanachama.

Alisema CALC inalenga kuimarisha uwezo wa wataalamu hao katika kuandaa sheria bora zinazotafsiri sera za Serikali na kuendana na mageuzi mbalimbali yanayohitajika katika nchi wanachama.

Aidha, chama hicho kinahamasisha ushirikiano katika mafunzo, kubadilishana uzoefu, programu za mafunzo kwa vitendo (attachments), matumizi ya teknolojia katika uandishi wa sheria pamoja na kuendeleza mbinu bora za taaluma hiyo.

“Lakini pia chama hiki kina Baraza la Uongozi linalojumuisha viongozi wakuu pamoja na wawakilishi kutoka mabara mbalimbali ambao ndio sisi tuliochaguliwa sasa. Kwa pamoja hushiriki katika kutoa mwelekeo na kufanya maamuzi kuhusu maendeleo ya taaluma ya uandishi wa sheria,” alisema Bi. Katuga.

Mwakilishi huyo wa Tanzania na Afrika alisema nafasi hiyo itamwezesha kuchangia kuimarisha ushirikiano wa wataalamu wa uandishi wa sheria nchini Tanzania na barani Afrika, kubadilishana maarifa na uzoefu na nchi nyingine za Jumuiya ya Madola, pamoja na kujifunza na kutumia mbinu bora za kisasa katika uandishi wa sheria.

Aidha, alisema anatarajia kushiriki kikamilifu katika kuunganisha wataalamu wa uandishi wa sheria barani Afrika, kukuza taaluma hiyo na kuchangia juhudi za kuboresha ubora wa sheria kupitia uandishi wenye weledi, uwazi na ufanisi.

Kwa Tanzania, uwakilishi huo unaongeza fursa ya kushiriki katika majadiliano ya kimataifa kuhusu maendeleo ya taaluma ya uandishi wa sheria na kunufaika na mafunzo, programu za kujengea uwezo wataalamu wa fani hiyo, pamoja na ubadilishanaji wa teknolojia na uzoefu. Hatua hiyo inatarajiwa kuchangia kuimarisha ubora wa mchakato wa uandaaji wa sheria nchini.

Matokeo ya uchaguzi huo yalitangazwa katika Mkutano Mkuu wa CALC uliofanyika tarehe 19 mwezi huu nchini Singapore.

Bayport Financial Services Tanzania imeadhimisha miaka 20 tangu kuanzishwa kwake kwa kutoa kompyuta 20 aina ya HP na mashine mbili za kuchapisha na kunakili (All-in-One Printers) zenye thamani ya jumla ya TZS milioni 100 kwa Idara ya Elimu ya Jimbo la Kibamba, ikiwa ni sehemu ya kuendeleza dhamira yake ya kusaidia sekta ya elimu na maendeleo ya taifa. 

Makabidhiano hayo yalifanyika rasmi katika hafla iliyofanyika katika Shule ya Msingi Anazaki, Kimara, na kuhudhuriwa na Mgeni Rasmi, Mheshimiwa Angellah Jasmine Kairuki, Mbunge wa Jimbo la Kibamba, pamoja na viongozi wa wilaya, maafisa wa elimu, wanahabari na wawakilishi wa Bayport.

 Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mkurugenzi Idara ya Mikopo Bayport Financial Services Tanzania, Amina Amani, alisema kuwa msaada huo ni sehemu ya juhudi za kampuni kuacha alama ya kudumu katika jamii wakati wa maadhimisho ya miaka 20 ya kuhudumia Watanzania.

 "Tulipotafakari namna bora ya kuadhimisha hatua hii muhimu, tulijiuliza ni kwa namna gani tunaweza kuacha urithi ambao utaendelea kuleta mabadiliko hata baada ya maadhimisho haya kuisha. Jibu lilikuwa wazi; tulitaka kufanya uwekezaji ambao utaendelea kuleta thamani kwa jamii na kuchangia safari ya maendeleo ya Tanzania kwa miaka mingi ijayo,"alisema Amani. 

Katika kipindi cha miaka 20 iliyopita, Bayport imehudumia zaidi ya Watanzania 430,439, wengi wao wakiwa watumishi wa umma, na kutoa mikopo yenye thamani ya zaidi ya TZS bilioni 529, iliyowasaidia wateja wake kutimiza malengo yao ya kifedha na maendeleo binafsi. 

Kompyuta na mashine za uchapishaji zilizotolewa zinatarajiwa kuimarisha mifumo ya usimamizi wa elimu kwa njia ya kidijitali katika Jimbo la Kibamba kwa kuongeza ufanisi wa kiutendaji, kuboresha utunzaji wa kumbukumbu na kuongeza upatikanaji wa teknolojia kwa maafisa wa elimu.

 "Kompyuta hizi ni zaidi ya vifaa vya teknolojia; ni fursa. Zitawawezesha maafisa wa elimu na walimu wanaojenga mustakabali wa taifa letu huku zikichangia kuboresha utoaji wa huduma kupitia mageuzi ya kidijitali," aliongeza Amani.

 Bayport imeeleza kuwa wakati Tanzania ikiendelea kutekeleza ajenda yake ya mageuzi ya kidijitali, upatikanaji wa teknolojia za kisasa ni muhimu katika kuboresha utoaji wa huduma za umma na kuandaa vizazi vijavyo kufanikiwa Katika uchumi wa kidijitali.

 Kampuni hiyo ilisisitiza kuwa mchango huo unaonesha dhamira yake ya kuwa taasisi inayowajibika kwa jamii na mshirika hai katika maendeleo ya taifa, mbali na jukumu lake la kutoa huduma za kifedha.

Bayport pia ilitoa shukrani kwa wateja wake, hususan watumishi wa umma wa Tanzania, ambao imani na ushirikiano wao vimewezesha ukuaji na mafanikio ya kampuni hiyo katika kipindi cha miongo miwili iliyopita.

 Mchango huu ni sehemu ya mpango wa Bayport wa Uwekezaji kwa Jamii (Corporate Social Investment) Katika maadhimisho ya miaka 20, unaolenga kuleta matokeo endelevu katika jamii zinazohudumiwa na kampuni hiyo.

 Akizungumza mara baada ya kupokea vifaa hivyo vya TEHAMA, Waziri Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Angellah Jasmine Kairuki ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Kibamba Mbunge wa Jimbo la Kibamba alisema kuwa msaada huo wa vifaa vya TEHAMA ni utekelezaji wa mkakati wa kuifanya Kibamba kuwa jimbo la kidijitali (Make Kibamba Digital) umeanza rasmi kwa kuimarisha matumizi ya teknolojia katika sekta ya elimu. 

Vifaa hivi vimekuja muda muafaka kwani vitarahisisha usimamizi wa elimu, mawasiliano kati ya idara mbalimbali, uratibu wa mitihani na utoaji wa huduma kwa walimu, wazazi na wanafunzi.

 “Tunaanza na idara za elimu, lakini huu ni mpango mpana wa kuifanya Kibamba kuwa jimbo la kidijitali. Tutaendelea kupeleka vifaa vya TEHAMA katika shule za sekondari, ofisi za kata na maeneo mengine ya huduma za umma kwa awamu,”amesema  Kairuki. 

Alibainisha kuwa tayari maandalizi yamekamilika kuzipatia shule za sekondari vifaa vya TEHAMA ikiwemo kompyuta, projectors na vifaa vingine vya kisasa, akisisitiza kuwa utekelezaji huo utafanyika hatua kwa hatua ndani ya kipindi cha miaka mitatu hadi minne. 

 Aidha, alitoa shukrani kwa Bayport Financial, pamoja na Idara ya Elimu ya Manispaa ya Ubungo kwa ushirikiano wao, akisema Bayport itaendelea kushirikiana na Serikali na jamii katika kutekeleza miradi yenye manufaa kwa wananchi.

Mkurugenzi Idara ya Mikopo Bayport Financial Services Tanzania, Amina Amani kulia akimkabidhi Waziri Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Angellah Jasmine Kairuki ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Kibamba, kumpyuta ya mezani kwa ajili ya Idara ya Elimu Jimbo la Kibamba. 

Bayport Financial Services Tanzania imeadhimisha miaka 20 tangu kuanzishwa kwake kwa kutoa kompyuta 20 aina ya HP na mashine mbili za kuchapisha na kunakili (All-in-One Printers) zenye thamani ya jumla ya TZS milioni 100 kwa Idara ya Elimu ya Jimbo la Kibamba, ikiwa ni sehemu ya kuendeleza dhamira yake ya kusaidia sekta ya elimu na maendeleo ya taifa. 


-Ni boti zinazotumia nusu saa Dar-Zanzibar ,Waziri Mkuu atoa maelekezo


Na Said Mwishehe,Michuzi TV

WAZIRI Mkuu Dk.Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuimarisha ulinzi na usalama katika Bahari na maziwa makuu ili kuhakikisha wanaofanya shughuli za kiuchumi katika maeneo hayo wanafanya kazi katika mazingira salama.

Akizungumza leo Julai 31,2026 katika viwanja vya bandari jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa boti za doria katika bahari na maziwa makuu,Dkt. Mwigulu amesema Serikali imeweka ulinzi na usalama kuwa kipaumbele cha maendeleo ya taifa.

"Niwaletee salamu za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye amenituma niwahakikishie kuwa Serikali itaendelea kuimarisha ulinzi na usalama katika maeneo ya maji ili wananchi wafanye shughuli zao kwa amani na usalama," amesema.

Ameongeza tayari Serikali imenunua vifaa vya kisasa vya uokoaji kwa Ziwa Victoria na sasa imeongeza uwezo wake kupitia uzinduzi wa boti mpya za doria zitakazosaidia kukabiliana na uhalifu na majanga katika bahari na maziwa.

Amefafanua hatua hiyo ni sehemu ya juhudi za Serikali kukabiliana na vitendo vya uhamiaji haramu, uharamia, usafirishaji wa dawa za kulevya, biashara haramu ya binadamu, uvuvi haramu, utoroshaji wa maliasili na unyang'anyi dhidi ya wavuvi.

“Mradi huu haujahusisha tu ununuzi wa boti za doria, bali pia umewezesha kuandaliwa kwa Mwongozo wa Kitaifa wa Kukabiliana na Uhalifu Baharini na Maziwani, kuanzishwa kwa Kituo cha Kitaifa cha Pamoja cha Operesheni, pamoja na kuwajengea uwezo wataalamu wa ndani kupitia mafunzo maalumu.”

Dk.Nchemba amesema usalama wa baharini ni muhimu kwa uchumi wa Tanzania kutokana na nafasi ya nchi kuwa lango la biashara kwa mataifa ya Afrika Mashariki na SADC.

"Kuimarika kwa usalama kutawapa wafanyabiashara na watumiaji wa Bandari ya Dar es Salaam uhakika zaidi wa kutumia lango letu la biashara," amesisitiza.

Aidha, ameagiza wizara na taasisi zote zinazohusika kutenga fedha za kutosha katika bajeti ya mwaka wa fedha 2027/28 kwa ajili ya uendeshaji, mafuta na matengenezo ya boti hizo ili zisikwame kutokana na ukosefu wa fedha.

Ametoa pia maelekezo kwa wasimamizi wa boti kuhakikisha zinafanyiwa matengenezo ya mara kwa mara na kutumika kwa kuzingatia miongozo ya kitaalamu.“Nazitaka wizara na taasisi zote zinazotakiwa kushiriki katika Kituo cha Kitaifa cha Pamoja cha Operesheni kupeleka wawakilishi wao ndani ya wiki mbili ili kituo hicho kianze kufanya kazi kikamilifu.

Pia ameishukuru Serikali ya Japan na Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo (UNDP), pamoja na washirika wengine wa maendeleo, kwa kufadhili mradi huo na kuahidi kuwa Serikali itaendelea kushirikiana nao katika kuimarisha usalama wa bahari na maendeleo ya uchumi wa buluu.

Kwa upande wake Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Profesa Palamagamba Kabudi amesema mradi huo umehusisha ununuzi wa boti mbili za doria, PB Sailfish II na PB Sailfish II, mafunzo kwa wataalamu wa kuzihudumia, pamoja na mradi ya kuwawezesha wakulima wa mwani katika Wilaya ya Mkinga, mkoani Tanga.

Ameongeza boti hizo zina uwezo wa kukimbia kwa kasi ya hadi knoti 50, sawa na takribani kilomita 92.6 kwa saa, hivyo kuongeza uwezo wa Serikali kufanya doria, kuzuia uhalifu baharini na kulinda rasilimali za bahari.”Spidi ya boti hizi zinatumia nusu saa kwenda Zanzibar na kurudi Dar.”

Awali akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Albert Chalamila, Mkuu wa Wilaya ya Ilala Edward Mpogolo amesema boti hizo ni utekelezaji wa Ilani ya CCM na juhudi za Serikali katika kuimarisha ulinzi na usalama pamoja na kukuza uchumi wa wananchi kupitia uchumi wa bluu.

“Boti hizi zitaongeza uwezo wa doria kuanzia Wilaya ya Kinondoni hadi Kigamboni, hivyo kuimarisha usalama wa wananchi na mali zao katika maeneo ya bahari.

Ameongeza boti hizo zitasaidia kudhibiti uvuvi haramu na kulinda rasilimali za bahari, hatua itakayowanufaisha wavuvi na wafanyabiashara wa samaki katika masoko ya Feri, Mbezi na Kigamboni.












Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Alhaj. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amejumuika na waumini wa Dini ya Kiislamu katika Ibada ya Sala ya Ijumaa iliyosaliwa katika Msikiti wa Jamiu Zinjibar, Mkoa wa Mjini Magharibi leo tarehe 31 Julai, 2026.

Baada ya Sala ya Ijumaa, Rais Dkt. Mwinyi ameshiriki Sala ya Jeneza ya Marehemu Sheikh Abdullah Hamid Suleiman, aliyekuwa Khatibu katika misikiti mbalimbali Zanzibar, iliyosaliwa katika Msikiti wa Jamiu Zinjibar.

Marehemu Sheikh Abdullah Hamid Suleiman, amefariki dunia leo, tarehe 31 Julai 2026, na kuzikwa kijijini kwao, Muungoni, Makunduchi, Mkoa wa Kusini Unguja.












Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo,akizungumza Julai 31, 2026 Jijini Dar es Salaam wakati akifungua Kikao cha Kamati Elekezi ya Programu ya Pili ya Kukuza Ujuzi na Stadi za Kazi (ESPJ II)

Na.Mwandishi Wetu.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo, amesema Programu ya Pili ya Kukuza Ujuzi na Stadi za Kazi (ESPJ II) ni hatua ya kimkakati inayolenga kuongeza ajira zenye tija na kuimarisha ustawi wa jamii.

Akizungumza Julai 31, 2026 Jijini Dar es Salaam wakati akifungua Kikao cha Kamati Elekezi ya Programu hiyo, Prof. Nombo amesema kuwa programu hiyo inalenga kuzalisha rasilimali watu wenye umahiri wa kisasa kwa sekta za viwanda, teknolojia, ubunifu na sekta binafsi, ili kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.

Prof. Nombo amebainisha kuwa Programu imeandaliwa katika misingi ya Mkakati wa Pili wa Taifa wa Kuendeleza Ujuzi, Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014 Toleo la 2023, pamoja na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Katibu Mkuu huyo amesisitiza kuwa matokeo makuu yanayotarajiwa ni kuongeza fursa za mafunzo kwa vijana wasio na ajira na wanaotoka katika mazingira magumu, kuimarisha mfumo wa kusimamia Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (TVET), na kushirikisha sekta binafsi katika kuboresha ubora wa mafunzo.

Kwa upande wake, Mratibu wa Programu ya Pili ya Kukuza Ujuzi na Stadi za Kazi, Dkt. Erick Mgaya, amesema utekelezaji wa Programu hiyo ni wa miaka sita wenye thamani ya Shilingi bilioni 780 sawa na Dola za Kimarekani milioni 300 unatarajiwa kunufaisha zaidi ya Watanzania milioni moja.

Amefafanua kuwa programu hii inatekelezwa na Taasisi 19 pamoja na wizara mbalimbali ikiwemo Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wizara ya Afya, Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI, Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano, pamoja na taasisi za mafunzo zikishirikiana na Sekta binafsi.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiagana na viongozi mbalimbali kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam kabla ya kuondoka nchini, kuelekea Luanda, Angola ambapo anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika hafla ya Uzinduzi wa Hospitali iliyopewa jina la Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, tarehe 31 Julai,2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Mama Maria Nyerere muda mfupi kabla ya kuanza safari ya kuelekea Luanda, Angola ambapo anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika hafla ya Uzinduzi wa Hospitali iliyopewa jina la Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, tarehe 31 Julai, 2026.

Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Mfumo wa Stakabadhi za Ghala umeendelea kuonyesha mafanikio makubwa nchini baada ya kuwawezesha wakulima na wazalishaji kuingiza zaidi ya Shilingi trilioni 2.2 kupitia mauzo ya mazao katika mwaka wa fedha 2025/2026, huku kiasi cha mazao yaliyouzwa kupitia mfumo huo kikiongezeka kwa asilimia 43.6 ikilinganishwa na mwaka uliopita.

Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari leo jijini Dodoma kuhusu utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) kwa mwaka wa fedha 2025/2026 na mwelekeo wa mwaka wa fedha 2026/2027, Mkurugenzi Mtendaji wa WRRB,  Asangye Bangu, amesema mafanikio hayo yanaakisi kuongezeka kwa imani ya wakulima na wadau katika matumizi ya mfumo huo.

Amesema Mfumo wa Stakabadhi za Ghala ulianza kutekelezwa kwa zao la korosho pekee, lakini kwa sasa umejumuisha mazao na bidhaa 18, ikiwemo kahawa, kakao, ufuta, soya, mbaazi, dengu, choroko, mahindi, mpunga, mchele, chai, maharage, karanga, asali, mihogo na vitunguu swaumu. Aidha, mfumo huo sasa unatekelezwa katika mikoa 23 nchini, hatua inayoonesha kupanuka kwa wigo wa huduma na kuimarika kwa masoko ya mazao.

 Bangu amesema katika mwaka wa fedha 2025/2026 Serikali ilitoa Shilingi milioni 950 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya WRRB. Fedha hizo zilielekezwa katika utoaji wa elimu na uhamasishaji kwa wakulima na wadau, uboreshaji wa miundombinu ya TEHAMA na mifumo ya kidijitali, kuimarisha ukaguzi na usimamizi wa maghala pamoja na ununuzi wa vitendea kazi vilivyoongeza ufanisi wa taasisi hiyo.

Ameeleza kuwa uwekezaji huo umeimarisha uwezo wa WRRB kusimamia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala kwa ufanisi zaidi na kuongeza upatikanaji wa huduma bora kwa wananchi.

Akifafanua mafanikio ya mfumo huo, amesema jumla ya kilo 1,122,246,475 za mazao tisa ambayo ni korosho, ufuta, kahawa, kakao, mbaazi, dengu, choroko, soya na chai ziliuzwa kupitia minada ya kidijitali inayosimamiwa na Soko la Bidhaa Tanzania (TMX), ikilinganishwa na kilo 781,659,285 zilizouzwa mwaka uliotangulia.

"Ongezeko hili la zaidi ya kilo milioni 340 ndani ya mwaka mmoja linaonesha kuwa wakulima wengi zaidi wanaendelea kuuamini Mfumo wa Stakabadhi za Ghala kutokana na uwazi, ushindani wa bei na uhakika wa soko unaopatikana kupitia mfumo huu," amesema.

Kutokana na mauzo hayo, wakulima na wauzaji walilipwa jumla ya Shilingi trilioni 2.298, huku Serikali za Mitaa zikikusanya Shilingi bilioni 61.05 kupitia ushuru wa mazao (CESS). Aidha, thamani ya biashara yote iliyofanyika kupitia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala ilifikia Shilingi trilioni 2.679.

 Bangu amesema fedha zilizowafikia wakulima zimechangia kuinua uchumi wa kaya kwa kuwawezesha kumudu gharama za elimu, afya, makazi na kuongeza uwekezaji katika shughuli za uzalishaji.

Aidha, amesema mapato yaliyopatikana kupitia ushuru wa mazao yameziwezesha Halmashauri kuimarisha utoaji wa huduma za jamii kwa kuwekeza katika ujenzi na ukarabati wa barabara, shule, vituo vya afya, masoko na miundombinu mingine muhimu inayowanufaisha wananchi.





NA DENIS MLOWE, IRINGA


WAKALA Mkuu wa mbegu za Taasisi ya ASA mkoani Iringa, Kampuni ya Mgongolwa Agrovet & Seeds Company Limited, imewahimiza wakulima kutumia mbegu bora zinazozalishwa na Taasisi ya ASA ili kuongeza uzalishaji wa mazao na kuondokana na changamoto ya kutumia mbegu zisizo na ubora.

Akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi za Iringa Press Club, Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Joseph Saidi Mgongolwa, alisema wamepewa dhamana na Taasisi ya ASA iliyo chini ya Wizara ya Kilimo kuhakikisha mbegu bora zinawafikia wakulima wa vijijini na mijini kwa wakati kabla ya kuanza kwa msimu wa kilimo.

Alisema hatua hiyo ni sehemu ya maandalizi kuelekea maadhimisho ya Siku ya Wakulima (Nanenane), huku lengo likiwa kuwafikishia wakulima mbegu zenye ubora wa hali ya juu kwa bei nafuu ili kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao.

Mgongolwa alisema Taasisi ya ASA imeamua kusogeza huduma karibu na wakulima kupitia mawakala wake ili kuhakikisha kila mkulima, mdogo na mkubwa, anapata mbegu bora zinazokidhi mahitaji ya maeneo mbalimbali ya kilimo nchini.
Alieleza kuwa kampuni hiyo itasambaza mbegu za mahindi zinazofaa kwa maeneo yenye mvua chache na maeneo yenye mvua nyingi, pamoja na mbegu za mpunga, alizeti na maharage ya njano na mekundu.

"Tunawaomba wakulima wa mkoa wa Iringa na Watanzania kwa ujumla kuamini mbegu za ASA ambazo zinazalishwa chini ya Wizara ya Kilimo. Mbegu hizi zimeonyesha uwezo mkubwa wa kuongeza mavuno na zinapatikana kwa bei nafuu ili kumwezesha mkulima kupata tija zaidi," alisema.

Aidha alisema kampuni hiyo imejipanga kufungua vituo vya usambazaji katika maeneo mbalimbali ya vijijini ili kurahisisha upatikanaji wa mbegu hizo, huku duka kuu likiwa katika eneo la CCM Mkoa wa Iringa.

Mgongolwa alisema moja ya changamoto kubwa iliyokuwa ikiwakabili wakulima ni uwepo wa mbegu feki, hali iliyosababisha wengi kupata hasara kutokana na mavuno hafifu.

Alisema kampuni yake itahakikisha mbegu zote zinazosambazwa ni halisi kutoka Taasisi ya ASA na zitakuwa na alama maalumu za utambuzi ikiwemo nembo ya Taifa ili kuondoa uwezekano wa wakulima kununua mbegu bandia.

"Nami ni mkulima na nimewahi kutumia mbegu mbalimbali baada ya kutumia mbegu za ASA nilishuhudia ongezeko kubwa la mavuno, ndiyo maana ninawahamasisha wakulima wenzangu kuzitumia kwa maendeleo ya kilimo chetu," alisema.

Kwa upande wa sifa za baadhi ya mbegu, alisema mbegu ya mahindi aina ya T105 hustawi katika maeneo yenye urefu wa mita 800 hadi 1,500 kutoka usawa wa bahari, hukomaa ndani ya siku 105 hadi 115 na inaweza kutoa magunia 18 hadi 22 kwa ekari endapo mkulima atazingatia kanuni bora za kilimo.

Aliongeza kuwa mbegu ya mpunga aina ya TXD 306 (Saro 5) imekusudiwa kwa maeneo ya mabondeni na skimu za umwagiliaji, hukomaa ndani ya siku 110 hadi 120, huku ikiwa na sifa ya kutoa mchele usiovunjika kirahisi wakati wa kukobolewa na wenye harufu nzuri.

Kwa mbegu ya alizeti aina ya Record, alisema hustawi katika maeneo yenye urefu wa mita 0 hadi 2,400 kutoka usawa wa bahari, hukomaa ndani ya siku 110 hadi 120 na inaweza kutoa mavuno ya kilo 600 hadi 800 kwa ekari, ikiwa na kiwango cha mafuta kati ya asilimia 32 na 48.

Mgongolwa alitoa wito kwa wakulima kutumia mbegu bora zilizoidhinishwa na serikali ili kuongeza uzalishaji wa mazao, kuimarisha usalama wa chakula na kuongeza kipato cha kaya kupitia kilimo chenye tija.



▪️Atoa siku 14 Kituo cha Kitaifa cha Oparesheni kianze kufanya kazi

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba ametoa siku 14 kwa wizara na taasisi zinazohusika na Kituo cha Kitaifa cha pamoja cha Oparesheni zipeleke wawakilishi ili kianze kufanya kazi mara moja.

"Wizara na taasisi zote zinazohusika na utekelezaji wa majukumu katika Kituo cha Kitaifa cha pamoja cha Oparesheni zipeleke wawakilishi wote wanaohitajika ndani ya siku 14 kuanzia leo. Kituo hiki kianze kazi mara moja ili kuleta tija inayokusudiwa," amesema Waziri Mkuu.

Dkt. Mwigulu ametoa wito huo leo (Ijumaa, Julai 31, 2026) wakati akizungumza na washiriki wa hafla ya makabidhiano na uzinduzi wa boti mbili za doria aina ya PB Sailfish 02 na PB Sailfish 03 iliyofanyika bandarini, jijini Dar es Salaam. Boti hizo zimenunuliwa kwa thamani ya dola za Marekani milioni 1.6.

Amezitaka Wizara za Muungano zinazohusika na suala hilo zishirikiane ili kuziba chochoro zote ambazo zingetumiwa na wahalifu katika eneo hili tunalolilenga na hasa katika mipaka ya mwambao wa bahari.

Ili kuhakikisha boti hizo zinafanya kazi kama inavyotarajiwa, Waziri Mkuu ameziagiza wizara na taasisi zote za umma zinazohusika katika matumizi ya boti hizi za doria zitenge fedha kwa ajili ya kazi za boti hizi.

"Ninasisitiza suala la kutenga bajeti ili kazi za doria zisikwamishwe na ukosefu wa bajeti. Nimekuwa nikikutana na kesi kama hizo mikoani ambapo Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan alinunua ambulance za kisasa na nyingine zina ICU lakini zinashindwa kuhudumia wagonjwa kwa wakati kwa kukosa mafuta. Hili linakinzana na dhamira njema ya Mheshimiwa Rais ya kutaka kuokoa maisha ya Watanzania pindi wanahitaji huduma hizo," amefafanua.

Akielezea umuhimu wa boti hizo za doria, Waziri Mkuu amesema makabidhiano ya boti hizo ni tukio muhimu kiuchumi kwa sababu zinaenda kulinda mazao yatokanayo na uchumi wa bluu. Amesema uhitaji wa boti hizo umekuwa ni kilio cha muda mrefu tangu yeye akiwa Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi.

Amesema upatikanaji wa boti hizo mbili, utaimarisha ulinzi hasa ikizingatiwa kwamba Tanzania ni lango la nchi nyingi zikiwemo za Afrika Mashariki na za SADC lakini usalama utakaokuwepo unahusu Tanzania na wananchi wa hizo nchi jirani. "Wananchi kutoka nchi hizo watakuwa na uhakika wa usalama watakapotumia lango la bandari ya Dar es Salaam," amesisitiza.

Mapema, akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na washiriki wa hafla hiyo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Prof. Palamagamba Kabudi alisema ununuzi wa boti mbili za doria aina ya PB Sailfish 02 na PB Sailfish 03 ulifanyika baada ya kukamilika kwa taratibu zote za manunuzi ambapo mkataba wa ununuzi ulisainiwa Julai 29, 2025 kati ya Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini na Kampuni ya Yamaha Motors Co. Ltd.

“Ujenzi wa boti hizo ulifanyika nchini Japan kwa kuzingatia vipimo na viwango vya kimataifa vilivyokubaliwa na wataalamu wa Serikali. Hadi kukamilika kwake, ujumbe wa wataalamu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, TASAC, UNDP na Chuo cha Mipango ulifanya ziara za ukaguzi ili kujiridhisha na ubora wa kazi iliyotekelezwa,” alisema.

Naye, Balozi wa Japan nchini Tanzania, Mikami Yoichi alisema kijiografia Tanzania na Japan ziko mbali lakini zinaunganishwa na bahari za Hindi na Pasifiki na kwamba uwepo wa usalama kwenye mipaka ya baharini, kuwahakikishia wananchi wake usalama wa maisha yao.

Alisema ana imani kwamba Serikali ya Tanzania itahakikisha boti hizo zinatumika kwa miaka mingi kwa faida ya vizazi vijavyo.













Top News