


Na OWM – TAMISEMI, Morogoro
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amewapongeza wakulima, wafugaji na wavuvi kwa mchango wao mkubwa uliowezesha Tanzania kufikia utoshelevu wa chakula wa zaidi ya asilimia 120, hatua inayodhihirisha mafanikio ya uwekezaji unaoendelea kufanywa na Serikali katika sekta za kilimo, mifugo na uvuvi.
Dkt. Mwigulu aliwasilisha pongezi hizo za Mhe. Rais Agosti 4, 2026, alipotembelea Maonesho ya Nane Nane Kanda ya Mashariki yanayofanyika katika Viwanja vya Nane Nane mkoani Morogoro.
Katika ziara hiyo alijionea shughuli na ubunifu wa wakulima, wafugaji na wavuvi kutoka mikoa ya Morogoro, Dar es Salaam, Pwani na Tanga.
Amesema maonesho ya mwaka huu yanaongozwa na kaulimbiu isemayo, "Tambua Soko; Ongeza Tija Kutekeleza Dira 2050," ambayo inawahimiza Watanzania kuzalisha kwa kuzingatia mahitaji ya soko, kutumia teknolojia za kisasa, kuongeza ubora wa bidhaa na kuimarisha mnyororo wa thamani ili kufanya kilimo kuwa biashara yenye tija na mchango mkubwa katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
"Kwa nilichojionea kupitia maonesho ya mwaka huu, ninaziona dalili zote kwamba ifikapo mwaka 2050 malengo ya Dira ya Taifa tuliyojiwekea yatakuwa yamefikiwa, kwa kuwa tuko kwenye hatua nzuri ya utekelezaji katika sekta za kilimo, mifugo na uvuvi," amesema Dkt. Mwigulu.
Ameongeza kuwa ameridhishwa na ubora wa mazao mbalimbali yaliyooneshwa, ikiwemo nyanya, bilinganya na bidhaa nyingine zinazokidhi viwango vya masoko ya kimataifa, yakiwemo ya Marekani na Ulaya, jambo linaloashiria kuwa Tanzania ipo kwenye mwelekeo sahihi wa kuzalisha bidhaa zenye ushindani duniani.
Akizungumzia sekta ya mifugo na uvuvi, Dkt. Mwigulu amesema zimeendelea kuwa nguzo muhimu za uchumi wa taifa, akibainisha kuwa mchango wa sekta ya mifugo katika pato la taifa umeongezeka kutoka asilimia 2.3 hadi asilimia 6.2.
Ametoa mfano wa mafanikio ya wanaonufaika na sekta hiyo kwa kumtaja kijana mmoja mhitimu anayejihusisha na ufugaji wa kisasa, ambaye ameonesha ng'ombe mwenye uzito wa zaidi ya kilogramu 1,000 mwenye thamani ya takribani Shilingi Milioni 20. Aidha, amesema kijana huyo anafuga zaidi ya ng'ombe 200 na alipoulizwa na Waziri wa TAMISEMI kama anahitaji mkopo, alieleza kuwa hana uhitaji huo kutokana na mafanikio ya shughuli zake.
Awali, akitoa neno la utangulizi kabla ya Waziri Mkuu kuzungumza na wananchi pamoja na washiriki wa maonesho hayo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, alisema Waziri Mkuu alimpa jukumu la ulezi wa Mkoa wa Morogoro, hivyo alimkaribisha rasmi kama waziri mwenyeji wa mkoa huo, ambao ni mmoja wa mikoa inayounda Kanda ya Mashariki katika Maonesho ya Nane Nane.
Jumla ya taasisi za umma 54 zinatarajiwa kuwasilisha taarifa za utendaji wa uwekezaji mbele ya Kamati za Kudumu za Bunge kwa muda wa wiki tatu, katika mchakato unaolenga kuwezesha uchambuzi wa thamani na utendaji wa mitaji ya umma pamoja na utekelezaji wa mipango ya kimkakati ya taasisi husika.
Katika awamu hii iliyoanza Jumatatu, Agosti 3, 2026, taasisi hizo zimepangwa kuwasilisha taarifa zao mbele ya Kamati mbili za Kudumu za Bunge, ambapo 27 zitawasilisha mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) na nyingine 27 mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Umma (PAC).
Hadi Jumatano, Agosti 5, 2026, taasisi nne zilikuwa tayari zimewasilisha taarifa zao mbele ya Kamati.
Taasisi hizo ni Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL), Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB), Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA) na Wakala wa Huduma za Ununuzi Serikalini (GPSA), huku Kamati zikionesha kuridhishwa na utendaji wa taasisi husika.
Uwasilishaji huo ni sehemu ya utekelezaji wa jukumu la kusimamia na kufuatilia utendaji wa uwekezaji wa Serikali kupitia taasisi na kampuni zilizo chini ya usimamizi wa Ofisi ya Msajili wa Hazina (OTR).
OTR inasimamia taasisi na kampuni 308, zikiwemo taasisi za umma 252 na kampuni 56 ambazo Serikali ina umiliki wa hisa chache, huku jumla ya uwekezaji katika taasisi na kampuni hizo ikiwa Sh92.3 trilioni.
Kaimu Msajili wa Hazina, Bi Lightness Mauki, alisema uwasilishaji huo unaipa Bunge fursa ya kupata picha ya kina kuhusu mwenendo wa uwekezaji wa mitaji ya umma.
“Uwasilishaji wa taarifa hizi ni moja ya utaratibu wa Bunge katika kusimamia Serikali, ikiwemo usimamizi wa uwekezaji wa mitaji ya umma,” alisema Bi. Mauki, ambaye pia ni Mkurugenzi wa Usimamizi wa Utendaji wa Mashirika ya Kibiashara.
Taarifa hizo huwezesha kuangalia thamani ya mitaji, mapato na matumizi, faida, hali ya mizania pamoja na utekelezaji wa mipango ya kimkakati ya taasisi husika, ikiwa ni msingi wa uwajibikaji na utawala bora,” alisema Mauki.
Uwasilishaji wa taarifa hizo unafanyika kwa mujibu wa Kanuni ya 11 ya Kanuni za Kudumu za Bunge, inayozipa Kamati jukumu la kuchambua na kubaini iwapo utekelezaji wa miradi ya uwekezaji wa umma unafanyika kwa ufanisi na kwa kuzingatia taratibu, sheria na miongozo ya biashara.
Kwa mujibu wa Bi. Mauki, Kamati pia inachambua na kujadili taarifa zinazohusu uwekezaji katika mashirika ya umma na kampuni ambazo Serikali inamiliki hisa.
Alisema OTR inaratibu mchakato huo na kuhakikisha taarifa zinazowasilishwa zinaakisi kwa usahihi na uwazi hali halisi ya utendaji wa taasisi na mashirika ya umma, ili kuwezesha Kamati za Bunge kufanya uchambuzi na kutoa ushauri na maelekezo yanayolenga kuimarisha utendaji.
“Jukumu la Ofisi ya Msajili wa Hazina katika zoezi hili ni kuratibu na kuhakikisha taarifa za mashirika ya umma zinakuwa na ukweli na uwazi wa hali halisi wa utendaji wa taasisi hizo ili kutoa fursa kwa Kamati za Bunge kushauri na kuelekeza katika masuala mbalimbali yanayolenga kuimarisha utendaji wa mashirika ya umma,” alifafanua Mauki.
Uwasilishaji wa taarifa za mashirika hayo ulitanguliwa na uwasilishaji wa Taarifa kuhusu hali ya Uwekezaji wa Umma hadi kufikia Mwaka 2024/2025 mbele ya PIC.
Taarifa hiyo, iliyowasilishwa na Bi. Mauki, ilijikita katika kuonesha hali ya uwekezaji wa Serikali ndani na nje ya nchi, mgawanyo wa uwekezaji katika mashirika ya umma, mapato yasiyo ya kodi ya mashirika na taasisi za umma, mikopo ya mashirika na taasisi za umma pamoja na taarifa za dhamana na misaada katika mashirika hayo.
Mchakato huo unaendelea kutoa fursa kwa Bunge kuchambua mwenendo wa uwekezaji wa mitaji ya umma na kutoa maoni na maelekezo yanayoweza kusaidia kuimarisha utendaji, uwajibikaji na matumizi yenye tija ya rasilimali za umma.
Elimu hiyo iliyotolewa katika ofisi za Ngorongoro ilijumuisha wadau muhimu wanaoguswa na mpango huo ambao ni viongozi wa jamii, wanafunzi pamoja na wadau mbalimbali ambao wamepewa uelewa kuhusu vigezo vya mkopo, sifa za waombaji pamoja na kupitia na kujadili mwongozo wa programu ya Ngorongoro Scholarship Fund.
Katika kikao hicho, viongozi wa jamii wamepongeza hatua ya Mamlaka ya kushirikiana na HESLB katika kuandaa na kuboresha mwongozo wa mfuko huo, wakieleza kuwa utasaidia kuweka utaratibu unaozingatia usawa, uwazi na mahitaji ya wakati katika kuwawezesha wanafunzi wenyeji kupata fursa za elimu ya juu.
Mwenyekiti wa Baraza la Wafugaji Ngorongoro, Mhe. Edward Maura, aliipongeza Mamlaka ya Ngorongoro na HESLB kwa kutoa elimu kuhusu Ngorongoro Scholarship Fund hasa jinsi wanufaika wanavyoweza kutambua fursa, kujaza fomu na kufuata taratibu za kuomba ufadhili.
“Tunawapongeza Ngorongoro na Bodi ya Mikopo kwa kutoa elimu hii kwa jamii na wanafunzi na kusaidia kuwaondolea wanafunzi changamoto na uelewa mdogo wa namna ya kuomba na kupata mikopo huu, tunaamini maamuzi haya ya Serikali yanalenga kuimarisha mahusiano kati ya jamii na Ngorongoro na tunaamini wanafunzi na jamii watatumia fursa zinazotolewa kwa kuzingatia taratibu zilizowekwa” alisema Mh. Maura.
Utekelezaji wa program hii unalenga kuimarisha ushirikiano na kuboresha huduma za jamii kwa wananchi wa Ngorongoro ambapo elimu wanayopata itasaidia ushiriki wao katika program za uhifadhi endelevu na kuvutia wageni kupitia vivutio vya utalii vilivyopo.
WALEZI wa watoto katika vituo vya kulelea watoto nchini wanatarajiwa kunufaika na mafunzo ya kitaalamu yatakayotolewa na Chuo cha Future World, hatua inayolenga kupunguza uhaba wa wataalamu wa malezi na makuzi ya awali ya watoto nchini.
Mwito huo umetolewa na Mkurugenzi wa Chuo cha Future World Institute Robert Mkolla katika mkutano wa wadau ulioandaliwa na Ofisa ustawi wa Jamii kanda ya saba Chanika Judith Mrema kwa kushirikiana na Umoja wa Vituo vya Kulea Watoto Tanzania (UVIKUWA), chini ya uratibu wa chuo cha ufundi stadi cha Future kilichopo Chanika kwa Ndevu, jijini Dar es Salaam.
“Mafunzo hayo yameandaliwa kujibu ongezeko la mahitaji ya walezi wenye taaluma, linalochochewa na kuongezeka kwa vituo vya kulelea watoto kutokana na mabadiliko ya kijamii na kiuchumi pamoja na kuongezeka kwa wazazi wanaojihusisha na shughuli za uzalishaji mali.”
Aidha, Mkolla amesema programu hiyo inaendana na Sera ya Elimu ya mwaka 2014, toleo la mwaka 2023, inayomtaka kila mtoto kupitia elimu ya awali kabla ya kuanza darasa la kwanza, jambo lililoongeza mahitaji ya huduma bora za malezi na makuzi ya awali.
Amefafanua mafunzo hayo yatawawezesha walezi kupata maarifa na stadi za kitaalamu kuhusu ukuaji wa mtoto, afya, usalama na elimu ya awali ili kuboresha huduma wanazozitoa.
Ameongeza programu hiyo pia itachangia kupunguza tatizo la ukosefu wa ajira kwa vijana, hususan wahitimu wa kidato cha nne, kwa kuwapatia ujuzi unaowawezesha kuajiriwa au kujiajiri katika sekta ya malezi ya watoto.
“Vituo vingi vya kulelea watoto bado vinategemea watu wasio na taaluma kutokana na uhaba wa wataalamu, hali inayoweza kuathiri ubora wa huduma zinazotolewa kwa watoto.”
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Umoja wa Vituo vya Kulea Watoto Tanzania (UVIKUWA Tanzania), Shabani Kibabi, amesem mafunzo hayo yataimarisha viwango vya malezi katika vituo vya kulelea watoto na kuchangia ustawi wa watoto kwa kuwawezesha walezi kupata ujuzi na taaluma stahiki.
Pia amesema katika mkutano huo umewajengea washiriki uwezo katika ujasiriamali na mbinu za kuongeza kipato, hatua itakayowasaidia kuboresha uendeshaji wa vituo vyao sambamba na utoaji wa huduma bora za malezi.
Kibabi amesema mbali na kozi ya malezi ya watoto, Chuo cha Future World kinatoa kozi nyingine zinazokidhi mahitaji ya soko la ajira, ikiwemo mafunzo ya kompyuta yanayochangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Naye Mwenyekiti wa UVIKUWA Mkoa wa Dar es Salaam, Muhina Mwarabu, amesema programu hiyo itasaidia kupunguza kwa kiasi kikubwa uhaba wa walezi wenye sifa katika vituo vya kulelea watoto.
Amewahimiza walezi pamoja na wamiliki wa vituo vya kulelea watoto kutumia fursa hiyo ya mafunzo, akisema ada ya Shilingi 800,000 ni nafuu na itawawezesha watu wengi zaidi kupata taaluma ya malezi ya watoto, hatua itakayoinua ubora wa huduma za malezi nchini.
Shirika lisilo la kiserikali la INADES-Formation Tanzania limesema linaendelea kutekeleza kauli mbiu ya Maonesho ya Kilimo Nanenane Kitaifa ya mwaka 2026 ya "Tambua Soko, Ongeza Tija, Tekeleza Dira ya Taifa 2050" kwa kuwawezesha wakulima na wafugaji kupata elimu ya kifedha, kuongeza uzalishaji na kuwaunganisha na masoko ya ndani na nje ya nchi kupitia bidhaa wanazozalisha.
Akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya Kilimo Nanenane Kitaifa yanayoendelea Jijini Dodoma, Mkurugenzi Mtendaji wa INADES-Formation Tanzania, Jacqueline Nicodemus, amesema shirika hilo limejikita katika kuhamasisha matumizi ya teknolojia rafiki kwa mazingira katika sekta za kilimo na ufugaji ili kuongeza tija na kuboresha maisha ya wananchi.
Amesema shirika hilo linalenga kuleta maendeleo ya kiuchumi kwa jamii za wakulima na wafugaji kwa kuwajengea uwezo wa kuzalisha kwa ufanisi, kuongeza thamani ya mazao na mifugo pamoja na kuwaunganisha na fursa mbalimbali za masoko.
Aidha, kwa sasa wamepanua wigo wa shughuli zao kwa kuhakikisha mkulima haishii kwenye uzalishaji wa mazao pekee, bali pia anashiriki katika shughuli za ufugaji ili kuongeza vyanzo vya kipato, ameongeza kuwa wanatoa mafunzo kwa njia ya masafa pamoja na vitabu na machapisho mbalimbali vinavyowasaidia wakulima na wafugaji kujifunza mbinu bora za uzalishaji na ufugaji wenye tija.
Aidha, amesema katika utekelezaji wa shughuli zake, INADES-Formation Tanzania imeendelea kuwekeza katika maeneo ya kilimo, ufugaji, hifadhi ya mazingira pamoja na kufungua fursa za kiuchumi katika wilaya, mikoa na vijiji mbalimbali kwa kushirikiana na mamlaka husika nchini.
Ameeleza kuwa kwa sasa INADES inafanya kazi katika mikoa ya Dodoma, Singida na Iringa, likihudumia jumla ya vijiji 26 na kuwafikia zaidi ya wananchi 150,000 kupitia vikundi vya wakulima, taasisi mbalimbali pamoja na wakulima mmoja mmoja.
Amesema ushiriki wa INADES-Formation Tanzania katika Maonesho ya Kilimo Nanenane unalenga kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu kilimo endelevu, ufugaji wenye tija, uhifadhi wa mazingira na matumizi ya teknolojia zinazoongeza uzalishaji huku zikiimarisha fursa za kiuchumi kwa jamii.
BENKI ya AbsaTanzania na Kampuni ya Knauf Gypsum Tanzania zimesaini Hati ya Makubaliano (MoU) ya kuanzisha Mpango wa Ufadhili kwa Wasambazaji (Distributor Financing Programme), hatua inayolenga kuwawezesha wasambazaji wa Knauf kupata mitaji ya biashara kwa urahisi zaidi, kuimarisha mnyororo wa ugavi na kuchochea ukuaji wa sekta ya ujenzi nchini.
Kupitia makubaliano hayo, Benki ya AbsaTanzania itatoa huduma maalum za kifedha kwa wasambazaji watakaokidhi vigezo vya benki, ikiwa ni pamoja na mikopo ya mtaji wa biashara na ufadhili wa ununuzi wa bidhaa. Awamu ya kwanza ya mpango huo inatarajiwa kuwahusisha wasambazaji kati ya 30 na 40 kutoka mtandao wa Knauf nchini Tanzania.
Akizungumza katika hafla ya utiaji saini iliyofanyika katika makao makuu ya Knauf Gypsum Tanzania jijini Dar es Salaam leo, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki AbsaTanzania, Bw. Obedi Laiser alisema, ushirikiano huo unaakisi dhamira ya benki hiyo ya kutumia huduma za kifedha kuimarisha biashara na kuongeza thamani katika mnyororo mzima wa biashara.
"Ushirikiano huu unaonesha nguvu ya mfumo shirikishi wa huduma za kibenki katika kusaidia ukuaji wa biashara na kuleta manufaa kwa wadau wote. Kwa kuwapatia wasambazaji wa Knauf suluhisho za kifedha, tunawawezesha kuongeza uwezo wao wa biashara, kuboresha ufanisi na kutumia kikamilifu fursa za ukuaji. Absa tunaendelea kutekeleza dhamira yetu ya kuiwezesha Afrika ya kesho, pamoja, hatua moja baada ya nyingine," alisema Bw. Laiser.
Alisema mpango huo utawapa wasambazaji uwezo wa kupata mitaji ya kuendesha biashara, kuongeza akiba ya bidhaa na kupanua shughuli zao, jambo litakaloimarisha upatikanaji wa bidhaa za Knauf katika soko la Tanzania.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Knauf Gypsum Tanzania, Bw. Christoforos Stamoulakatos, alisema ushirikiano huo utawajengea uwezo wasambazaji wa kampuni hiyo na kuongeza ufanisi wa huduma kwa wateja.
"Wasambazaji wetu ni sehemu muhimu ya mafanikio ya kampuni yetu na uwezo wetu wa kuwahudumia wateja kote nchini. Kupitia ushirikiano huu na Absa Bank Tanzania, tunawapa fursa ya kupata huduma za kifedha zitakazowasaidia kukuza biashara zao na kukidhi mahitaji yanayoendelea kuongezeka sokoni," alisema.
Mpango huo unaendana na mkakati wa Benki ya Absa Tanzania wa mfumo shirikishi wa huduma za kibenki unaolenga kutoa huduma jumuishi za kifedha zinazosaidia mnyororo mzima wa thamani kwa kuwaunganisha wazalishaji, wasambazaji na wadau wengine wa biashara kupitia suluhisho bunifu za kifedha.
Knauf Gypsum Tanzania ni mmoja wa wateja wakubwa wa Benki ya Absa Tanzania katika kitengo cha Wateja wa Makampuni (CIB), na kampuni hiyo imeendelea kuwa mdau muhimu katika sekta ya ujenzi nchini. Kupitia mpango huo mpya, taasisi hizo zinatarajia kuimarisha zaidi ushirikiano wao na kufungua fursa mpya za ukuaji wa biashara kwa wadau wote.
Hafla ya utiaji saini ilihudhuriwa na viongozi wakuu wa Benki ya Absa Tanzania na Knauf Gypsum Tanzania, wasambazaji, washirika wa biashara pamoja na wawakilishi wa vyombo mbalimbali vya habari.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw Obedi Laiser (kulia), na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Knauf Gypsum Tanzania, Bw. Christoforos Stamoulakatos, wakisaini Hati za Makubaliano (MoU) yenye lengo la kuanzisha Mpango wa Ufadhili kwa Wasambazaj, hatua inayolenga kuwawezesha wasambazaji wa Knauf kupata mitaji ya biashara kwa urahisi zaidi, kuimarisha mnyororo wa ugavi na kuchochea ukuaji wa sekta ya ujenzi nchini. Hafla hiyo ilifanyika jijini Dar es Salaam leo. Kushoto ni Meneja wa Sheria na Mahusiano ya Nje na Serikali wa Knauf, Bi. Flora Erasto na kulia ni Katibu wa Kampuni kutoka Benki ya Absa Tanzania, Bw. Desmond Malyi.















.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)




.jpeg)





.jpeg)





.jpeg)




