Na Mwandishi wetu Dodoma

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amewapongeza wenyeviti na wajumbe wa tume zilizoundwa kutathmini matumizi ya ardhi katika eneo la Ngorongoro Conservation Area kwa kazi kubwa na ya kizalendo waliyoifanya katika kukamilisha majukumu yao.

Rais Samia amesema hayo leo Machi 12, 2026 katika Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma wakati akipokea ripoti za tume hizo, akisema jukumu walilopewa lilikuwa zito kutokana na kuhusisha maoni ya wadau wengi wenye mitazamo tofauti.

Amesema licha ya changamoto hizo, wenyeviti na wajumbe wa tume walitekeleza kazi yao kwa bidii, uadilifu na weledi mkubwa, hali iliyowezesha kukusanywa kwa taarifa muhimu zitakazosaidia kufanya maamuzi sahihi kwa manufaa ya taifa.

Rais Samia amesema baada ya kusikiliza kwa kina taarifa za tume hizo pamoja na kutazama makala ya video iliyoonesha hali halisi ya maeneo yaliyotembelewa, imebainika umuhimu wa kulinda mfumo wa ikolojia unaounganisha maeneo ya Ngorongoro Conservation Area, Pololeti Game Reserve na Lake Natron.

Amesema mfumo huo wa ikolojia ni wa kipekee na una umuhimu mkubwa kwa uhifadhi endelevu wa mazingira pamoja na rasilimali za taifa.

Aidha, Rais Samia amesema taarifa hizo pia zimeonesha uwepo wa rasilimali mbalimbali ikiwemo madini yanayotafutwa duniani ambayo yanapatikana katika maeneo hayo, hivyo kusisitiza umuhimu wa kuyahifadhi kwa manufaa ya taifa na dunia kwa ujumla.

Katika hatua nyingine, Rais Samia amesema taarifa za tume pia zimeonesha changamoto zilizojitokeza katika utekelezaji wa zoezi la uhamaji wa hiari kwa wakazi wa eneo la Ngorongoro kwenda maeneo ya Msomera, Saunyi na maeneo mengine.

Amesema Serikali ilianza zoezi hilo kwa nia njema, lakini imebaini kuwa kulikuwa na mapungufu katika baadhi ya maeneo, hivyo ni muhimu kuyatafakari na kuyarekebisha kabla ya kuendelea na hatua zinazofuata.

Rais Samia amesisitiza kuwa Serikali itaendelea na zoezi hilo la uhamaji wa hiari, lakini kwa kufanya maboresho yatakayozingatia changamoto zilizobainishwa ili kuhakikisha utekelezaji wake unakuwa bora na wenye manufaa kwa wananchi pamoja na taifa.






Kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Sahara Ventures, Jumanne Mtambalike na kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa DTBi, Patience Abraham, wakionesha mikataba ,ara baada ya kusaini kuashiria ushirikiano wakukuza programu ya kitaifa ya kuharakisha ukuaji wa biashara changa 1000 na kuimarisha mfumo wa ubunifu nchini, uzinduzi huo umefanyika leo Machi, 12, 2026.. katikati ni  Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH, Dkt. Amos Nungu.
Kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Sahara Ventures, Jumanne Mtambalike na kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa DTBi, Patience Abraham wakibadilishana mikataba mara baada ya kuzindua programu maalumu inayolenga kusaidia zaidi ya kampuni changa 1,000 nchini kukua na kujiimarisha kibiashara katika kipindi cha miaka minne ijayo. Uzinduzi huo umefanyika leo Machi 12, 2026 jijini Dar es Salaam.

Na Mwandishi Wetu.
TUME  ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) kwa kushirikiana na Sahara Ventures kupitia vituo vya ubunifu vya Dar Teknohama Business Incubator (DTBi) na Buni Innovation Hub imezindua programu maalumu inayolenga kusaidia zaidi ya kampuni changa 1,000 nchini kukua na kujiimarisha kibiashara katika kipindi cha miaka minne ijayo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa programu hiyo jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH, Dkt. Amos Nungu, amesema mpango huo unalenga kuimarisha mfumo wa ubunifu nchini kwa kuwapa vijana fursa ya kubadilisha mawazo yao ya kibunifu kuwa biashara zenye tija kwa uchumi wa taifa.

“Tanzania ina vijana wengi wenye mawazo ya ubunifu, lakini changamoto imekuwa ni namna ya kuyaendeleza mawazo hayo hadi kufikia soko. Kupitia programu hii tunataka kuwasaidia vijana kupata msaada wa kitaalamu, mitaji na fursa za kuunganisha wabunifu na wawekezaji,” amesema Dkt. Nungu.

Ameeleza kuwa kupitia mpango huo takribani kampuni changa 250 zitapatiwa msaada kila mwaka, hatua itakayosaidia kufikisha zaidi ya kampuni changa 1,000 kunufaika na mafunzo ya biashara, ushauri wa kitaalamu pamoja na fursa za masoko.

Kwa mujibu wa Dkt. Nungu, programu hiyo itajikita katika sekta sita muhimu ambazo ni nishati safi, madini na rasilimali za uchimbaji, utalii na huduma za ukarimu, kilimo na mifugo, viwanda pamoja na teknolojia za kisasa.

“Lengo letu ni kujenga mfumo imara wa ubunifu kwa kuunganisha vyuo vikuu, watafiti, wajasiriamali na wawekezaji ili kuhakikisha mawazo ya ubunifu yanageuzwa kuwa bidhaa na huduma zinazochochea maendeleo ya kiuchumi,” ameongeza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Sahara Ventures, Jumanne Mtambalike, amewataka vijana wenye mawazo ya kibunifu au wanaomiliki kampuni changa kujitokeza kuomba kushiriki katika programu ya Tanzania Ventures Lab inayotekelezwa chini ya ushirikiano huo.

“Tunawahamasisha vijana kuwasilisha maombi yao kupitia tovuti ya https://tanzaniaventureslab.co.tz/ kwaajili ya kujisajili pamoja na kupata fursa ya mafunzo, ushauri wa kitaalamu na kuunganishwa na wawekezaji watakaosaidia kukuza biashara zao,” amesema Mtambalike.

Ameongeza kuwa programu hiyo inalenga kuwajengea vijana uwezo wa kutumia ubunifu na teknolojia katika kukuza biashara zao na kuchangia maendeleo ya uchumi wa taifa.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa DTBi, Patience Abraham, amesema kitengo hicho kilicho chini ya COSTECH kimejipanga kuendelea kuwasaidia vijana kukuza ubunifu na kubadilisha mawazo yao ya kibunifu kuwa biashara zinazoweza kuleta tija katika uchumi.

“DTBi itaendelea kutoa mafunzo, ushauri wa kitaalamu pamoja na mazingira wezeshi yatakayosaidia kampuni changa kukua na kujitegemea katika sekta mbalimbali za kimkakati,” amesema Patience

Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH, Dkt. Amos Nungu akizungumza jijini Dar es Salaam leo wakati wa uzinduzi rasmi programu ya kitaifa ya kuharakisha ukuaji wa biashara changa 100o na kuimarisha mfumo wa ubunifu nchini, uzinduzi huo umefanyika leo Machi, 12, 2026. kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Sahara Ventures, Jumanne Mtambalike na kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa DTBi, Patience Abraham.

Kushoto niMkurugenzi Mtendaji wa Sahara Ventures, Jumanne Mtambalike akizungumza jijini Dar es Salaam leo wakati wa uzinduzi rasmi programu ya kitaifa ya kuharakisha ukuaji wa biashara changa 1000 na kuimarisha mfumo wa ubunifu nchini, uzinduzi huo umefanyika leo Machi, 12, 2026. 
Mkurugenzi Mtendaji wa DTBi, Patience Abraham akizungumza jijini Dar es Salaam leo wakati wa uzinduzi rasmi programu ya kitaifa ya kuharakisha ukuaji wa biashara changa 1000 na kuimarisha mfumo wa ubunifu nchini, uzinduzi huo umefanyika leo Machi, 12, 2026. 


Matukio mbalimbali katika picha.

SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) Kanda ya Magharibi imefanikiwa kutoa leseni 129 kwa wazalishaji wa bidhaa katika kanda hiyo, huku leseni 99 kati ya hizo zikitolewa kwa wajasiriamali wadogo.

Akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mafanikio ya TBS katika sekta ya viwanda, Meneja wa TBS wa Kanda hiyo, Bw. Hamisi Seleleko amesema hatua hiyo inaonesha jitihada za shirika hilo katika kuwasaidia wazalishaji kufuata viwango vinavyotakiwa na hivyo kuimarisha ubora wa bidhaa zinazozalishwa nchini.

Amesema mafanikio hayo pia yametokana na mahusiano mazuri kati ya TBS na Tawala za Mikoa, Wilaya pamoja na Halmashauri katika kanda hiyo, hali iliyosaidia kuimarisha ukaguzi na utekelezaji wa sheria.

Kutokana na ushirikiano huo, wananchi wamekuwa wakipatiwa elimu ya viwango mara kwa mara jambo ambalo limechangia kupungua kwa bidhaa hafifu sokoni, hususan za chakula na vipodozi.

Bw. Seleleko amesema kiasi cha bidhaa hafifu kilichokamatwa kimepungua kutoka tani 11 mwaka 2024 hadi kufikia tani 8 mwaka 2025.

Aidha, amesema TBS Kanda ya Magharibi imefanikiwa kusajili majengo zaidi ya 2,100 ya chakula na vipodozi, ikilinganishwa na mwaka 2020 wakati ofisi hiyo ilipofunguliwa ambapo majengo 400 pekee ndiyo yaliyokuwa yamesajiliwa.

Amesema hatua hiyo inaonesha kuongezeka kwa uelewa wa wazalishaji na wafanyabiashara kuhusu umuhimu wa kuzingatia viwango katika uzalishaji wa bidhaa ili kulinda afya na usalama wa watumiaji.
  


Tume ya Ushindani (FCC) imesema wazalishaji wa vifaa vya ujenzi wana wajibu wa kumlinda mlaji kwa kuhakikisha wanazalisha na kuuza bidhaa zenye ubora unaolingana na thamani ya fedha anayolipa mnunuzi.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa semina kwa wazalishaji wa vifaa vya ujenzi kuelekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Mlaji Duniani yenye kauli mbiu isemayo "Bidhaa Salama, Imani kwa Mlaji", Mkurugenzi wa Udhibiti wa Mienendo ya Bidhaa Inayokatazwa na Sheria ya Ushindani wa FCC, Bi. Magdalena Utouh, kwa niaba ya Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, amesema ulinzi wa mlaji ni miongoni mwa majukumu makuu ya Tume hiyo.

FCC imeeleza kuwa suala la usalama wa bidhaa za ujenzi si suala la biashara pekee, bali ni suala la usalama wa jamii na maendeleo ya Taifa kwa ujumla hivyo ni muhimu kwa wazalishaji kuzingatia viwango vinavyotakiwa katika uzalishaji wa vifaa vya ujenzi ili kuepusha uwepo wa bidhaa zisizo na ubora sokoni, ambazo zinaweza kusababisha hasara kwa watumiaji na kudhoofisha imani ya wananchi katika bidhaa hizo.

Amesema FCC itaendelea kufuatilia mwenendo wa soko la bidhaa za ujenzi ili kuhakikisha haki za walaji zinalindwa na wananchi wanapata bidhaa salama na zenye ubora unaokidhi viwango vinavyotakiwa.
Bi. Utouh amewataka wazalishaji wa vifaa vya ujenzi kuendesha biashara zao kwa kuzingatia sheria na kanuni za ushindani wa haki, hatua ambayo itasaidia kujenga soko lenye ushindani wa kweli unaolinda maslahi ya walaji pamoja na kuchochea maendeleo ya sekta ya ujenzi nchini.

Ameeleza kuwa sekta ya ujenzi ni mhimili muhimu wa ukuaji wa uchumi wa taifa, hivyo uzalishaji wa vifaa vya ujenzi unapaswa kufanyika kwa kuzingatia viwango stahiki na thamani halisi ya fedha inayolipwa na mlaji.

“FCC ina jukumu la kufuatilia mwenendo wa ushindani katika soko ili kuhakikisha hakuna makubaliano ya kupanga bei miongoni mwa wafanyabiashara ambayo yanaweza kumuathiri mlaji,” amesema Bi.Magdalena
 
Amesema Tume haitavumilia vitendo vyovyote vinavyomuumiza mlaji, akisisitiza kuwa sheria na miongozo ya ushindani ipo wazi na wazalishaji wanapaswa kuizingatia kikamilifu.

Hata hivyo amesema mikutano na majadiliano kati ya FCC na wadau wa sekta ya ujenzi itaendelea kufanyika mara kwa mara ili kuimarisha ushindani wa soko na kuhakikisha walaji wanapata bidhaa na huduma bora.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Huduma za Wanachama wa Shirikisho la Wamiliki wa Viwanda Tanzania (CTI), Bi. Neema Mhondo, amesema sekta ya ujenzi ina mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa nchi pamoja na kutoa ajira kwa wananchi.

Hata hivyo, amesema wazalishaji wa ndani wanakabiliwa na changamoto ya uwepo wa bidhaa bandia sokoni, hali inayofanya viwanda vya ndani kupata ugumu katika ushindani kutokana na gharama kubwa za uzalishaji na uendeshaji wa biashara.

Semina hiyo ya siku moja imefanyika Machi 11, 2026 katika Ukumbi wa Mikutano wa Ngorongoro katika Ofisi za FCC, Jijini Dar es Salaam. 
Mkurugenzi wa Udhibiti wa Mienendo ya Bidhaa inayokatazwa na Sheria ya Ushindani wa FCC Bi.Magdalena Utouh akizungumza wakati akifungua Semina ya Wadau wa Uzalishaji wa Vifaa vya Ujenzi ,jijini Dar es Salaam.
















 

Morogoro, Tanzania, 10 March 2026: Miaka ya hivi karibuni, magonjwa yasiyoambukiza yanaendelea kuwa changamoto kubwa kwa afya ya jamii nchini Tanzania. Magonjwa kama shinikizo la damu, kisukari, magonjwa ya moyo pamoja na saratani yanaongezeka kwa kasi, huku wengi wakigundulika wakiwa tayari katika hatua za mwisho za ugonjwa kutokana na kukosekana kwa uchunguzi wa mapema na uelewa mdogo kuhusu kinga na dalili zake.

Kwa mujibu wa takwimu za afya nchini, magonjwa yasiyoambukiza yanachangia takribani asilimia 34 ya vifo vyote nchini Tanzania, jambo linaloonyesha umuhimu wa kuimarisha juhudi za kinga, uchunguzi wa mapema pamoja na elimu kwa jamii kuhusu namna ya kujikinga na magonjwa hayo.

Kwa jamii nyingi, hasa zile zilizo mbali na huduma za afya au zenye changamoto za kifedha, watu wengi huchelewa kufanya uchunguzi wa afya hadi pale hali inapokuwa mbaya zaidi. Hali hii huongeza hatari za kiafya ambazo zingeweza kuzuilika kupitia uchunguzi wa mapema na ushauri wa kitaalamu.

Kwa kutambua umuhimu wa kukabiliana na changamoto hii, sekta binafsi zimeendelea kushirikiana na serikali katika kuboresha upatikanaji wa huduma za afya kwa jamii. Katika kuunga mkono juhudi hizi, Vodacom Foundation Tanzania imeanza zoezi la Kambi ya Matibabu ya Bure kwa ajili ya uchunguzi wa magonjwa yasiyoambukiza kwa wakazi wa Morogoro, ikilenga kuwasogezea wananchi huduma muhimu za uchunguzi, ushauri na elimu ya afya.

Baada ya kufanikisha kambi ya afya ya bure iliyofanyika hivi karibuni Zanzibar iliyohudhuriwa na zaidi ya wananchi 2000 waliopata huduma mbali mbali za uchunguzi wa afya na ushauri wa kitabibu, sasa mpango huo unaelekea Morogoro ili kuwafikia wananchi wengi zaidi.

Kwa kushirikiana na madaktari bingwa kutoka Muhimbili National Hospital, Vodacom Tanzania Foundation inaleta tena huduma za uchunguzi na matibabu bila malipo ili kusogeza huduma muhimu za afya karibu zaidi na wananchi.

Kambi hiyo ya afya itafanyika katika Viwanja vya Shule ya Kilosa Mjini mkoani Morogoro, kuanzia tarehe 10 hadi 13 Machi 2026, ambapo wananchi watapata huduma mbalimbali za uchunguzi ikiwemo shinikizo la damu, kisukari, magonjwa ya moyo pamoja na ushauri wa kitaalamu kuhusu namna ya kujikinga na kudhibiti magonjwa yasiyoambukiza.

Mpango huu ni sehemu ya juhudi za muda mrefu za Vodacom Tanzania Foundation katika kusaidia jamii kupitia huduma za afya, elimu na miradi mingine ya maendeleo, huku ukilenga kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa uchunguzi wa mapema na kinga dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza.

Akizungumza Katika hafla hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Kilosa, Shaka Hamdu Shaka, alipongeza Vodacom Tanzania Foundation pamoja na Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa kuandaa makambi haya ya afya yanayotoa huduma bure kwa wananchi wa Kilosa.

“Tunapenda kuishukuru Vodacom Tanzania Foundation na Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa kuwa mdau muhimu katika sekta ya afya na kwa kuendelea kuleta huduma hizi karibu zaidi na wananchi. Kambi hii ya huduma za afya imeandaliwa kwa kuzingatia jiografia ya eneo hili pamoja na mahitaji halisi ya wananchi’

Akielezea kuhusu mpango huo, Meneja wa Vodacom Tanzania Foundation, Sandra Oswald, alisema kuwa afya bora ya jamii ni msingi muhimu wa maendeleo ya taifa.

“Afya njema ndiyo msingi wa jamii yenye nguvu na tija. Kupitia kambi hizi za matibabu bure tunalenga kuwahamasisha wananchi kuchukua hatua za mapema kuhusu afya zao kwa kufanya uchunguzi, kupata ushauri wa kitaalamu na kujifunza njia bora za kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza,” alisema.

Aliongeza kuwa Vodacom Tanzania Foundation itaendelea kushirikiana na wataalamu wa afya pamoja na wadau mbalimbali kuhakikisha huduma za kinga na uchunguzi wa magonjwa yasiyoambukiza zinawafikia wananchi wengi zaidi, hususan wale wanaokabiliwa na changamoto za kifedha au umbali wa huduma za afya.

Mpango huu pia unaendana na malengo ya maendeleo endelevu ya kimataifa, hususan Sustainable Development Goal 3 yanayolenga kuhakikisha afya bora na ustawi kwa wote.

Vodacom Tanzania Foundation inawahimiza wakazi wa Morogoro kujitokeza kwa wingi katika kambi hiyo ili kufanyiwa uchunguzi wa afya na kupata elimu kuhusu namna ya kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza, kwani uchunguzi wa mapema na uelewa sahihi ni hatua muhimu katika kujenga jamii yenye afya bora na mustakabali imara.







Balozi wa Tanzania nchini Zimbabwe, Kamishna wa Polisi (CP) Suzan Kaganda, amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi wa Idara ya Afrika na Asia katika Wizara ya Mambo ya Nje na Biashara za Kimataifa ya Zimbabwe, Bw. Mqabuko Dube.

Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika nchini Zimbabwe, viongozi hao walijadili masuala mbalimbali ya ushirikiano kati ya Tanzania na Zimbabwe, hususan katika kuimarisha mahusiano ya kidiplomasia na ushirikiano wa kikanda.

Aidha, pande zote mbili zilikubaliana kuendeleza na kuimarisha ushirikiano uliopo kati ya nchi hizo mbili, pamoja na kushirikiana kwa karibu katika utekelezaji wa majukumu yao kwa lengo la kuchochea maendeleo ya pamoja na kuimarisha uhusiano wa kirafiki uliopo kati ya Tanzania na Zimbabwe.

Na Mwandishi Wetu, Arusha.

Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela kwa kushirikiana na Taasisi ya Global Education Link Ltd wamesaini hati ya makubaliano ya ushirikiano yenye lengo la kukuza tafiti, ubunifu na maendeleo ya kisayansi.

Makubaliano hayo yatakayosaidia kuandaa kizazi kipya kitakacholeta mapinduzi ya kiuchumi na kiteknolojia Barani Afrika na duniani kwa ujumla.

Ushirikiano huo unatarajiwa kufungua milango ya fursa mpya katika sekta ya elimu, utafiti na ubunifu, pamoja na kuitangaza taasisi hiyo kimataifa ili dunia itambue kuwa Tanzania ina taasisi inayozalisha vipaji na teknolojia za kisasa kupitia ushirikiano na vyuo vikuu mbalimbali vya nje ya nchi.

Akizungumza mara baada ya kusainiwa kwa makubaliano hayo, Makamu Mkuu wa Taasisi ya Nelson Mandela, Profesa Maulilio Kipanyula, alisema Afrika ina hazina kubwa ya vipaji ambavyo vikisimamiwa na kupangwa vizuri vinaweza kutoa suluhisho la changamoto mbalimbali zinazoikabili jamii.

Profesa Kipanyula alisisitiza kuwa ubunifu na maendeleo ya kisayansi hayawezi kufikiwa bila ushirikiano wa taasisi mbalimbali, akibainisha kuwa makubaliano hayo ni hatua muhimu katika kuongeza idadi ya wanafunzi, hususan wanafunzi wa kimataifa, pamoja na kuchangia kukuza uchumi.

Alisema makubaliano hayo ni ya kimkakati katika kuhakikisha elimu inayotolewa inaendelea kuimarika kimataifa kwa kuvutia vipaji vya vijana kusoma na kuwasilisha bunifu zao kupitia Taasisi ya Nelson Mandela.

Aidha, alieleza kuwa anatamani kuona taasisi hiyo ikiendelea kuzalisha na kulea vipaji vya vijana pamoja na ubunifu mbalimbali utakaosaidia kuchochea maendeleo katika majukwaa ya kitaifa na kimataifa.

“Tunataka tafiti zetu na matokeo yake yawafikie wananchi kwa haraka zaidi, ambapo ubunifu na maarifa vitakuwa na mchango mkubwa kwa jamii. Utafiti na ubunifu lazima viwe na uwezo wa kutatua changamoto za watu,” alisema Profesa Kipanyula.

Naye Mkurugenzi wa Taasisi ya Global Education Link Ltd, Abdullmalik Mollel, alisema ushirikiano huo umejikita katika kuimarisha masuala ya kitaaluma, uwekezaji na matumizi ya teknolojia ili kuongeza tija katika sekta ya elimu na uchumi.

Alisema elimu inayotolewa kwa wanafunzi inapaswa kuwa na mchango wa moja kwa moja katika kukuza uchumi na maendeleo kwa kutumia teknolojia, maarifa na mitaji.

“Elimu anayopewa mwanafunzi inapaswa kusaidia kukuza uchumi na kuleta maendeleo kupitia teknolojia, maarifa na uwekezaji. Ushirikiano wa maarifa kati ya vyuo vikuu mbalimbali utaongeza tija katika kukuza uchumi unaotegemea teknolojia,” alisema Mollel.

Aliongeza kuwa makubaliano hayo ni mwanzo wa safari ya ushirikiano wa muda mrefu kati ya taasisi hizo mbili, wenye lengo la kuimarisha ushirikiano wa vyuo vikuu na kuleta mabadiliko chanya katika sekta ya elimu, utafiti na maendeleo ya jamii kwa ujumla.








Shirika lisilo la kiserikali la Kikristo ECHO East Africa kutoka Ngaramtoni jijini Arusha limefanya warsha ya mafunzo kwa vitendo kwa waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali vya habari jijini Arusha kuhusu Kilimo Ikolojia (Agroecology).

Shirika hilo linafanya kazi katika nchi za Afrika Mashariki pamoja na baadhi ya nchi za Kusini mwa Afrika, Lengo ni kuwasaidia wakulima, hususan wakulima wadogo, kwa kuwapatia mbinu mbadala, elimu, ujuzi na maarifa ili kuongeza uzalishaji wa mazao yao kwa kutumia mbinu rafiki kwa mazingira, ikiwemo kilimo ikolojia.

Warsha hiyo ya mafunzo kwa vitendo imefanyika kwa siku mbili na Dhumuni la mafunzo hayo ni kuwaleta pamoja waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali ili kuwafahamisha juu ya uwepo wa shirika hilo, kuelewa shughuli mbalimbali zinazotekelezwa, pamoja na kuwapa elimu kuhusu kilimo ikolojia.

Katika mafunzo hayo, waandishi wa habari wamepata fursa ya kufanya ziara katika maeneo mbalimbali ndani ya shirika hilo na kujifunza masuala kadhaa ya kilimo ikolojia. Miongoni mwa mambo waliyojifunza ni pamoja na mbinu za uvunaji wa maji ili kupunguza mmomonyoko wa udongo, kilimo mseto, upandaji wa miti, na matumizi ya mazao yanayofunika ardhi ili kulinda rutuba ya udongo.

Aidha, washiriki wametembelea miradi mbalimbali inayotekelezwa na shirika hilo, ikiwemo benki ya mbegu, uzalishaji wa biogas, matumizi ya mitambo ya kukaushia vyakula, pamoja na kutembelea wakulima ambao ni wanufaika wa mbinu za kilimo ikolojia.

Kilimo Ikolojia (Agroecology) ni mfumo wa kilimo unaochanganya kanuni za ikolojia, yaani mazingira ya asili, na uzalishaji wa mazao. Lengo lake ni kuzalisha chakula kwa njia rafiki kwa mazingira, endelevu na yenye kunufaisha wakulima pamoja na jamii kwa muda mrefu.

Wataalamu wa kilimo wanaendelea kuhamasisha matumizi ya kilimo ikolojia kama njia mbadala ya kuongeza uzalishaji wa chakula huku wakilinda mazingira. Mbinu hii inahusisha matumizi ya rasilimali za asili, kupanda mazao mchanganyiko, pamoja na kupunguza utegemezi wa kemikali shambani.






Top News