Na Oscar Assenga,TANGA.
'
Zaidi ya wananchi 20,000 kutoka kaya masikini mkoani Tanga wameanza kunufaika na mpango wa Bima ya Afya kwa Wote, unaolenga kuboresha upatikanaji wa huduma za matibabu kwa kaya zenye kipato cha chini.

Mpango huo, unaotekelezwa kwa awamu ya kwanza na ya pili, unalenga kuwafikia wananchi walio katika mazingira magumu kiuchumi ili kuwawezesha kupata huduma za afya bila kikwazo cha gharama za matibabu. Ufadhili wa mpango huo unatolewa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF), ukiwa na lengo la kupunguza mzigo wa gharama za matibabu kwa kaya masikini.

Hadi sasa, zaidi ya wanufaika 20,000 kutoka kaya 7,816 wamepatiwa kadi za bima ya afya na wameanza kutumia huduma hizo tangu Machi mwaka huu. Hatua hiyo imeelezwa kuwa imeleta matumaini mapya kwa wananchi wengi ambao hapo awali walikabiliwa na changamoto ya kumudu gharama za matibabu.

Akizungumza katika Maonesho ya Kibiashara ya Mwahako, Daktari Lawi Kupaza kutoka Mfuko wa Bima ya Afya (NHIF) Mkoa wa Tanga amesema mwitikio wa wananchi umekuwa mkubwa, huku wengi wa walengwa waliostahili tayari wakikabidhiwa kadi zao.

Amesema zoezi hilo linaendelea vizuri katika halmashauri zote za mkoa huo, huku awamu ya pili ikitarajiwa kufikia kaya nyingine 1,300.

“Kwa sasa tunaendelea na ugawaji wa kadi pamoja na uhakiki wa taarifa za wanufaika. Tunawahamasisha wananchi kujitokeza kuhakiki taarifa zao ili waweze kupata huduma kwa wakati,” amesema Dkt. Kupaza.



Hata hivyo, amekiri kuwepo kwa changamoto ya kuwafikia wanufaika wote kwa wakati kutokana na ukubwa wa maeneo ya utekelezaji na ratiba za shughuli mbalimbali.

“Kuna changamoto ya kuwafikia wanufaika wote kwa wakati kutokana na ratiba na ukubwa wa eneo la utekelezaji. Hata hivyo, watendaji wa kata na vijiji wanaendelea kusaidia katika uhamasishaji,” ameongeza.



Kwa upande wake, Afisa Madai wa NHIF, Neema Kisinga, ameitaka jamii kuendelea kujiunga na bima ya afya ili kujikinga na gharama kubwa za matibabu.

Amesema mfuko huo una vifurushi mbalimbali vinavyowezesha wananchi kupata huduma za afya kwa gharama nafuu, ikiwemo kifurushi cha Tarangire ambacho kinatoa huduma za matibabu, vipimo na ushauri wa daktari kwa gharama nafuu kwa mwaka mzima.



“Kuwa na bima ya afya kunapunguza mzigo wa kulipia huduma kila unapougua au kuhitaji matibabu. Hii ni njia bora ya kujilinda na gharama zisizotarajiwa za afya,” amesema Kisinga.

Mpango huo unaendelea kuonekana kama hatua muhimu katika juhudi za Serikali za kuhakikisha wananchi wote, hususan wa kipato cha chini, wanapata huduma bora za afya bila kuathiriwa na changamoto za kifedha.
Na Ashura Mohamed – Arusha

Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amewataka wasomi na watafiti nchini kuja na suluhisho la kudumu la kumaliza ugonjwa wa Malaria, kama ambavyo wasomi katika mataifa mengine wamefanikiwa kuutokomeza ugonjwa huo.

Akizungumza Jijini Arusha wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa 33 wa Kisayansi wa Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR), Waziri Mchengerwa alisema wataalamu ni lazima waje na tafiti mbalimbali zitakazosaidia jamii kuondokana na changamoto za kiafya.

“Ndugu zangu watafiti, ugonjwa wa Malaria ni lazima sasa ifike mwisho. Wapo wanaotumia dawa lakini haziwasaidii, lakini mazingira yao yapoje? Wapo wanaotumia vyandarua, lakini je watavitumia mpaka maeneo ya kutafuta biashara zao? Hilo si kweli. Au tutatumia njia gani na utaalam gani kumaliza mazalia ya mbu katika mazingira yao? Wajibu wa watafiti ni kuleta suluhisho. Au tukibuni suluhisho taasisi zetu zitakosa kipato? Tuambizane tu,” alisema Mchengerwa.

Aidha, Waziri Mchengerwa alisema haiwezekani changamoto ya Malaria ambayo imedumu kwa miaka zaidi ya mia moja bado iendelee kusumbua nchi zinazoendelea, wakati katika mataifa makubwa duniani ugonjwa huo umekwisha na kuwa historia licha ya kuanzia katika mataifa hayo.

“Ni vema tukakubaliana kuwa maamuzi magumu mtayatafiti katika kipindi hiki. Nikiwa Waziri, tutamshauri Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuyatekeleza ili ugonjwa wa Malaria utokomezwe kabisa. Haiwezekani kila siku tunalia Malaria wakati kuna mataifa Malaria kwao ni historia. Twende tukaokoe vifo vya mama na watoto wachanga chini ya miaka mitano kwa kutokomeza ugonjwa wa Malaria,” alisisitiza Waziri.

Pia alisema anaamini NIMR ikiwezeshwa itapiga hatua katika tafiti mbalimbali, kwa kuwa yapo maeneo yanayoweza kusubiri ila si tafiti.

Alibainisha kuwa mara nyingi fedha zinazotengwa kwa ajili ya tafiti haziwafikii kwa wakati, hali inayokwamisha maendele huku akisisitiza kuwa ili taifa lipige hatua, utafiti haukwepeki.

“Eneo la tafiti kwenye nchi yetu halikwepeki. Tukifanikiwa kwenye tafiti na wenzetu wa mipango wakitusaidia kutafsiri, nchi itapiga hatua kubwa sana, kwa kuwa changamoto zilizopo kwenye jamii zitapata majibu,” alisema.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Taasisi ya Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu(NIMR), Profesa Aboud alisema taasisi hiyo imeendelea kufanya tafiti zinazotegemea ushahidi wa kisayansi na kusaidia uundaji wa sera bora za afya.

Alitaja tafiti zilizochangia mabadiliko ya sera ya chanjo ya saratani ya shingo ya kizazi kutoka dozi mbili hadi dozi moja, pamoja na tafiti za kifua kikuu zinazoonesha uwezekano wa kupunguza muda wa matibabu kutoka miezi sita hadi miezi minne kwa manufaa ya Serikali na wagonjwa.
Waziri wa Afya Mohamed Mchengerwa akizungumza na Watafiti katika Kongamano la 33 la Kisayansi lilioanza Leo Mkoani Arusha


Na Janeth Raphael MichuziTv 

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI, kupitia kwa Mwenyekiti wake Johanes Lukumay, ameipongeza Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) kwa mafanikio makubwa katika utoaji wa huduma za kibingwa na ubobezi, akisema hospitali hiyo imeendelea kuwa tegemeo muhimu kwa wananchi wanaohitaji matibabu ya kiwango cha juu nchini.

Lukumay ametoa pongezi hizo baada ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI kufanya ziara katika hospitali hiyo jijini Dodoma, ambapo ilikagua maendeleo ya ujenzi wa Jengo la Matibabu ya Saratani, kutembelea wagonjwa pamoja na kujionea huduma mbalimbali zinazotolewa na hospitali hiyo.

Akizungumza baada ya ziara hiyo, Lukumay amesema uongozi wa BMH chini ya Mkurugenzi Mtendaji, Profesa Abel Makubi, umeonyesha mfano wa uongozi bora kwa kuhakikisha wananchi wanapata huduma za afya zenye ubora wa hali ya juu.

“Hospitali hii ilianza kutoa huduma za upandikizaji wa uloto mwaka 2023. Hadi sasa watoto 30 tayari wamefanyiwa huduma hiyo kwa mafanikio, jambo ambalo linaonyesha uwezo mkubwa wa kitaalamu uliopo hapa,” alisema Lukumay.

Ameongeza kuwa kati ya watoto hao 30, watoto 20 walipatiwa gharama za matibabu kupitia msaada wa Samia Suluhu Hassan, hatua aliyosema imechangia kwa kiasi kikubwa mafanikio ya huduma hiyo muhimu kwa watoto wenye mahitaji maalum ya matibabu.

“Tunapaswa kuipongeza Hospitali ya Benjamin Mkapa kwa kazi kubwa inayofanya katika kuokoa maisha ya Watanzania na kuendelea kupanua huduma za kibingwa na ubobezi,” alisisitiza.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Afya, Florence Simizi, alimpongeza Rais Samia kwa uwekezaji mkubwa unaoendelea kufanyika katika hospitali hiyo, ambao umeiwezesha kuimarisha huduma za afya kwa wananchi.

Amesema kuelekea maadhimisho ya miaka 10 tangu kuanzishwa kwa hospitali hiyo, serikali imeendelea kushuhudia mafanikio makubwa katika utoaji wa huduma za afya.

“Tumekuja kujionea maendeleo yaliyopo hapa. Hospitali hii kwa sasa inatoa huduma 20 za kibingwa na huduma 17 za ubobezi. Hili si jambo dogo kwa sababu huduma hizi zinahitaji wataalamu wa kada mbalimbali pamoja na miundombinu ya kisasa,” alisema Dkt. Simbazi.

Ameongeza kuwa utoaji wa huduma hizo unategemea uwepo wa miundombinu bora, vifaa tiba vya kisasa na wataalamu wenye ujuzi wa hali ya juu, mambo ambayo yameendelea kupewa kipaumbele na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa BMH, Profesa Makubi, amesema hospitali hiyo inaendelea kutekeleza mipango mbalimbali ya maendeleo yenye lengo la kuifanya kuwa kituo kikuu cha matibabu nchini.

Amesema moja ya maono ya hospitali hiyo ni kuona BMH ikifikia hadhi ya Hospitali ya Taifa, huku maeneo ya wazi yanayozunguka hospitali yakitumika kuanzisha “Kijiji cha Matibabu” kitakachojumuisha huduma mbalimbali za afya na uwekezaji katika sekta ya tiba.

Profesa Makubi ameeleza kuwa hatua hiyo itachochea maendeleo ya sekta ya afya, kuongeza upatikanaji wa huduma za kibingwa na ubobezi, pamoja na kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha huduma za matibabu katika ukanda wa Afrika Mashariki.












Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Dkt. Jabiri K. Bakari, amewataka watumishi wa Mamlaka hiyo kuendana na mabadiliko kwa kujenga utamaduni wa kupanga, kubuni, kushirikiana na kuwahusisha wadau katika utekelezaji wa majukumu yao, akieleza kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kuimarisha utendaji wa taasisi na kuchochea maendeleo endelevu ya sekta ya usafiri wa anga nchini.

Dkt. Bakari alitoa rai hiyo wakati wa mafunzo maalum ya siku nne yaliyofanyika katika Chuo cha Uongozi cha Mwalimu Julius Nyerere, Kibaha, kuanzia Juni 5 hadi 8, yaliyowakutanisha viongozi na wawakilishi wa watumishi wa TCAA kutoka vituo mbalimbali nchini.

Mafunzo hayo yalitoa fursa kwa washiriki kutafakari utendaji wa Mamlaka, kujadili vipaumbele vya kimkakati na kubaini njia bora za kuimarisha utoaji wa huduma pamoja na ufanisi wa taasisi kwa ujumla.

Sehemu ya kwanza ya mafunzo ilijikita katika maendeleo binafsi na ujenzi wa timu kupitia programu iliyoendeshwa na Peak Performance. Kupitia shughuli mbalimbali za ndani na nje ya darasa, washiriki walishiriki mazoezi yaliyolenga kuimarisha mshikamano, kujenga kuaminiana, kuboresha mawasiliano na kuhamasisha mabadiliko chanya ya fikra na mtazamo.

Washiriki walihamasishwa kutafakari upya namna wanavyotekeleza majukumu yao, kujenga nidhamu binafsi, kuzingatia afya na ustawi wa mwili pamoja na kuendeleza tabia zinazochangia mafanikio ya mtu mmoja mmoja na taasisi kwa ujumla. Mafunzo hayo pia yalisisitiza umuhimu wa kujitambua, uwajibikaji na kuwa na mtazamo chanya katika kufanikisha malengo ya pamoja.

Moja ya matokeo muhimu ya mafunzo hayo ilikuwa kuandaliwa kwa waraka wa pamoja wa kujenga timu (Team Building Charter) unaoakisi maadili, matarajio na dhamira ya pamoja iliyojengwa wakati wa mafunzo hayo. Waraka huo unatarajiwa kuwa mwongozo wa kuimarisha utamaduni wa taasisi, kukuza ushirikiano na uwajibikaji, pamoja na kusaidia juhudi za Mamlaka katika kufikia ubora wa utendaji na utoaji huduma.

Katika kipindi chote cha mafunzo, washiriki pia walijadili masuala mbalimbali ya kimkakati ikiwemo utendaji wa Mamlaka, mipango ya bajeti, michakato ya kazi, ushirikishwaji wa wadau na fursa za kuboresha utoaji wa huduma. Majadiliano hayo yalitoa nafasi kwa viongozi na watumishi kutathmini changamoto zilizopo, kubaini fursa na kujadiliana kuhusu suluhisho zitakazosaidia kuimarisha ufanisi wa Mamlaka.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, Dkt. Bakari alisisitiza umuhimu wa kuondokana na utamaduni wa kushughulikia matatizo baada ya kutokea na badala yake kujenga utamaduni wa kupanga, kufanya tafiti na kufanya maamuzi kwa kuzingatia taarifa sahihi na ushahidi.

Aliwataka watumishi kutumia tafiti, takwimu na taarifa za wakati halisi katika kuelewa mwenendo wa sekta na kufanya maamuzi yatakayosaidia kuimarisha huduma na kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa majukumu ya Mamlaka.

Mkurugenzi Mkuu huyo pia alisisitiza umuhimu wa kuzingatia dhana ya “Know Your Customer” (KYC) kwa kuwafahamu kwa kina wadau wa sekta ya anga, kuelewa mahitaji yao na kujenga mahusiano mazuri yatakayowezesha utoaji wa huduma bora zaidi.

“Lazima tuwafahamu wateja na wadau wetu, tuelewe changamoto zao na mazingira wanayofanyia kazi. Uelewa mzuri wa wadau wetu utatuwezesha kufanya maamuzi sahihi, kuboresha utoaji wa huduma na kuchangia kwa ufanisi maendeleo ya sekta ya usafiri wa anga,” alisema.

Dkt. Bakari alisisitiza pia umuhimu wa kujenga na kuendeleza mahusiano imara na wadau mbalimbali wa sekta ya anga, akieleza kuwa ushirikiano, kuaminiana na mawasiliano endelevu ni nguzo muhimu katika kuhakikisha sekta hiyo inaendelea kukua kwa usalama, ufanisi na ushindani.

Aidha, aliwataka watumishi kufuatilia kwa karibu mwenendo wa sekta, kufanya tafiti na kutumia taarifa mbalimbali katika kuelewa changamoto na mahitaji ya wadau ili kusaidia kufanya maamuzi yenye tija kwa maendeleo ya sekta.

Kwa upande mwingine, Dkt. Bakari alisisitiza umuhimu wa afya na ustawi wa watumishi, akibainisha kuwa taasisi yenye watumishi wenye afya njema, ari ya kazi na mtazamo chanya ndiyo yenye uwezo mkubwa wa kufanikisha malengo yake. Aliwahimiza watumishi kuzingatia afya zao za mwili na akili ili kuwa na nguvu na uthabiti wa kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Mafunzo hayo yalihitimishwa kwa washiriki kubaini suluhisho za changamoto mbalimbali za kiutendaji na kuthibitisha upya dhamira yao ya kuimarisha ushirikiano, ubunifu, ushirikishwaji wa wadau na utoaji wa huduma bora.

Majadiliano yaliyofanyika yanaakisi dira ya TCAA ya kujenga taasisi yenye utendaji wa hali ya juu inayoweza kuendelea kuisimamia na kuiendeleza sekta ya usafiri wa anga kwa usalama, ufanisi na kwa kuzingatia mahitaji ya wadau wake.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Dkt. Jabiri K. Bakari akizungumza wakati wa mafunzo maalum ya siku nne ya kuimarisha utendaji wa taasisi na kuchochea maendeleo endelevu ya sekta ya usafiri wa anga nchini yaliyofanyika katika Chuo cha Uongozi cha Mwalimu Julius Nyerere, Kibaha mkoani Pwani.






Baadhi ya watumishi wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) wakiwa kwenye mafunzo ya kuimarisha utendaji wa Taasisi hiyo.

WAZIRI wa Viwanda na Biashara Judith Kapinga, amesema Serikali imeendelea kuweka mazingira bora ya uwekezaji na biashara kwa kuboresha sera, sheria na mifumo ya utoaji huduma kuvutia uwekezaji wenye tija.

Kapinga ameyasema hayo jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa chapa mpya ya magari Jetour, jijini Dar es Salaama, ambapo amefafanua uzinduzi huo unaendana kikamilifu na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mpango wa Tatu wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano na Ajenda ya Taifa ya Ujenzi wa Uchumi wa Viwanda na Biashara.

Ameongeza uwekezaji huo unadhihirisha dhamira ya kukuza ushiriki wa sekta binafsi, kuongeza matumizi ya rasilimali za ndani,uhamishaji wa teknolojia na kuzalisha ajira kwa Watanzania.

"Tunatambua Africarriers na Jetour hawaleti magari pekee nchini bali wanaleta fursa mpya za biashara, uwekezaji, ajira, maarifa ya kiteknolojia na mchango mkubwa katika maendeleo ya uchumi wa Tanzania na ukanda wetu wa Afrika Mashariki,”amesema Waziri Kapinga.

Pia amewapongeza viongozi wa Africarriers Group na Jetour Global kwa maono yao makubwa kuichagua Tanzania kuwa sehemu ya safari yao ya ukuaji na mafanikio huku akisisitiza Serikali itaendelea kushirikiana na wawekezaji wote wenye nia ya dhati ya kuchangia maendeleo ya Taifa letu.

Akieleza zaidi amesema ujio wa Jetour nchini Tanzania kunafungua ukurasa mpya wa fursa za kiuchumi na uwekezaji huo utazalisha ajira mpya kwa vijana katika maeneo mbalimbali yakiwemo ya mauzo, huduma za kiufundi, ushauri wa huduma kwa wateja, teknolojia ya habari na mawasiliano pamoja na huduma nyingine.

Waziri Kapinga amesema pia mafanikio ya Africarriers kwa kipindi cha zaidi ya miaka 50 ni ushahidi wa uwezo, uthubutu na ustahimilivu wa wafanyabiashara wa Kitanzania.

“Kupitia ushirikiano huo na Jetour, watapiga hatua nyingine muhimu kuelekea Tanzania yenye viwanda imara, ajira nyingi, biashara shindani na uchumi jumuishi kwa kizazi cha sasa na vizazi vijavyo.”

Kwa upande wa Mkuu wa Idara ya Sheria wa Kampuni za Africarries, Ngasa Mboje amesema kwa mara ya kwanza wameleta gari zinazoendana na soko na mahitaji ya Watanzania kwasababu ni gharama nafuu.

“Magari ya Jetour yanauzwa kwa njia ya malipo ya papo kwa hapo na njia ya mpili ni kwa mkopo kwasababu kuna baadhi ya Watanzania hawawezi kumudu gharama kwa mara kwanza.Hivyo unaweza kununua kwa mkopo na kulipa kidogo kidogo, huku ukiendelea kulitumia gari lako.”
Mgeni rasmi Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe.Judidh Salvio Kapinga akizungumza mbele ya Wageni waalikwa mbalimbali waliofika kwenye hafla ya uzinduzi rasmi wa Chapa mpya ya Magari ya Jetour nchini Tanzania,iliofanyika Juni 8,2026 Masaki, jijini Dar es Salaam

Balozi wa Shirikisho la Urusi nchini Tanzania Mhe. Andrey Avetisyuan akizungumza mbele ya Wageni waalikwa mbalimbali waliofika kwenye hafla ya uzinduzi rasmi wa Chapa mpya ya Magari ya Jetour nchini Tanzania,iliofanyika Juni 8,2026 Masaki, jijini Dar es Salaam,ambapo mgeni rasmi alikuwa ni Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe.Judidh Salvio Kapinga
Makamu wa Rais wa Kampuni ya Magari ya Africarriers Group,Bw. Shahid Nabi, akizungumza mbele ya Wageni waalikwa mbalimbali waliofika kwenye hafla ya uzinduzi rasmi wa Chapa mpya ya Magari ya Jetour nchini Tanzania,iliofanyika Juni 8,2026 Masaki, jijini Dar es Salaam,ambapo mgeni rasmi alikuwa ni Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe.Judidh Salvio Kapinga
Baadhi ya Viongozi na wageni waalikwa wakishuhudia uzinduzi wa Chapa mpya ya Magari ya Jetour nchini Tanzania,hafla iliofanyika Juni 8,2026 Masaki, jijini Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa Makampuni ya Africarriers, Bw. Fida Rashid, akimkabidhi Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania, Mhe. Chen Mingjian mfano wa gari ya Jetour iliozinduliwa nchin Tanzania.
Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania, Mhe. Chen Mingjian akiwasha gari ya Jetour iliozinduliwa nchini Tanzania hapo jana,Masaki jijini Dar es Salaam.
Picha ya pamoja mara baada ya uzinduzi wa Chapa mpya ya Magari ya Jetour nchini Tanzania,hafla iliofanyika Juni 8,2026 Masaki, jijini Dar es Salaam.






Na Janeth Raphael, MichuziTv

Watanzania wanatarajia kupata burudani ya hali ya juu ya soka la kimataifa baada ya Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) kutangaza rasmi kuwa litarusha mubashara Michuano ya Kombe la Dunia la FIFA 2026 bila malipo.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Juni 9, 2026 jijini Dodoma, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TBC, Upendo Mbelle, amesema shirika hilo limefanikiwa kupata haki rasmi za kurusha mashindano hayo makubwa ya dunia yatakayofanyika kuanzia Juni 11 hadi Julai 19, 2026 katika mataifa ya Marekani, Mexico na Canada.

Amesema Watanzania wataweza kufuatilia mashindano hayo kupitia televisheni ya TBC, redio, pamoja na majukwaa ya mtandaoni ikiwemo Facebook, YouTube, Instagram na TikTok, sambamba na tovuti rasmi ya shirika hilo.

“Tumejipanga kuhakikisha Watanzania wanapata matangazo ya ubora wa juu, yakiambatana na uchambuzi wa kina kutoka kwa wachambuzi wenye uzoefu mkubwa wa soka,” amesema Mbelle.

Ameongeza kuwa uzoefu wa muda mrefu wa TBC katika kurusha matukio makubwa ya michezo, tangu enzi za Radio Tanzania Dar es Salaam (RTD), umeiwezesha shirika hilo kuendelea kutoa huduma bora kwa watazamaji na wasikilizaji wake.

Kwa mujibu wa Mbelle, mchezo wa ufunguzi wa Kombe la Dunia 2026 utapigwa Juni 11, 2026, ukiwakutanisha wenyeji Mexico dhidi ya Afrika Kusini, ambapo TBC itakuwa tayari kuurusha mubashara kuanzia dakika ya kwanza.

Aidha, amesema TBC imeweka kaulimbiu maalum ya “Pira Mtelezo”, ikilenga kuwaletea Watanzania burudani ya kipekee ya soka la kimataifa wakiwa majumbani au walipo popote.

Upendo Mbelle amesisitiza kuwa TBC imewahi kurusha pia matoleo ya Kombe la Dunia ya mwaka 2010 Afrika Kusini, 2014 Brazil, 2018 Urusi na 2022 Qatar, jambo linaloonyesha uzoefu wake mkubwa katika utangazaji wa mashindano ya kimataifa.

Pia amebainisha kuwa katika kipindi cha hivi karibuni, TBC imeendelea kuimarisha uwezo wake kupitia kurusha michuano mikubwa kama CHAN 2025 iliyofanyika Tanzania, Kenya na Uganda pamoja na AFCON 2025 iliyofanyika Morocco.

“Tunaendelea kujipanga kuhakikisha kila Mtanzania anapata nafasi ya kushuhudia soka la kiwango cha juu duniani kupitia chombo chake cha habari anachokiamini,” ameongeza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Masoko wa TBC, Daphrosa Kimbory, amesema shirika hilo limejipanga kikamilifu kulinda haki zake za matangazo, akisisitiza kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya yeyote atakayekiuka makubaliano ya haki miliki.

Naye Mkuu wa Dawati la Michezo TBC, Evance Muhando, amesema TBC inaendelea kuwa nyumbani kwa wachambuzi na watangazaji wengi wa soka nchini, na amewakaribisha Watanzania kufurahia mashindano hayo mubashara kupitia chombo hicho cha umma.




Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) inatarajia kuandika historia mpya Julai 1, 2026 kwa kuadhimisha miaka 30 tangu kuanzishwa kwake, huku Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, akitarajiwa kutoa Tuzo Maalum za Rais kwa Walipakodi Bora kwa mwaka wa fedha 2024/2025.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma Juni 9, 2026 kwa niaba ya Kamishna Mkuu wa TRA, Mkurugenzi wa Elimu kwa Mlipakodi na Mawasiliano, Richard Kayombo, amesema maadhimisho hayo yatafanyika chini ya kaulimbiu isemayo; “Miongo Mitatu ya TRA, Mlipakodi Shujaa, Tanzania Inayojitegemea.”

Kayombo ameeleza kuwa maadhimisho hayo yataambatana na shughuli mbalimbali za kitaifa na kikanda zitakazoanza kabla ya kilele chake Julai 1, 2026, kwa lengo la kuendelea kuimarisha ukusanyaji wa mapato ya Serikali, kuboresha huduma kwa walipakodi na kuhamasisha ulipaji kodi kwa hiari.

Amefafanua kuwa shughuli hizo zitahusisha vipindi maalum vya elimu ya kodi kupitia redio, televisheni na majukwaa ya kidijitali, kliniki za kodi, huduma za ushauri kwa walipakodi, mikutano na wadau mbalimbali wakiwemo wafanyabiashara, wahasibu na washauri wa kodi pamoja na ziara za kuwafikia walipakodi katika maeneo mbalimbali nchini.

Aidha, maadhimisho hayo yataenda sambamba na utoaji wa Tuzo ya Rais kwa Walipakodi Bora, hatua inayolenga kutambua na kuthamini mchango wa walipakodi walioonyesha uadilifu, uwajibikaji na uzalendo katika kulipa kodi na kuchangia maendeleo ya taifa.

Kwa mujibu wa Kayombo, tuzo hizo zinalenga kuimarisha utamaduni wa ulipaji kodi na kutuma ujumbe kwamba kulipa kodi si wajibu wa kisheria pekee, bali ni kitendo cha uzalendo na ushiriki wa moja kwa moja katika kujenga Tanzania yenye uchumi imara, huduma bora za kijamii na fursa zaidi kwa wananchi.

Ikumbukwe TRA ilianzishwa kwa Sheria ya Bunge mwaka 1995 na kuanza rasmi shughuli zake Julai 1, 1996, ikiwa na jukumu la kusimamia ukusanyaji wa kodi na mapato mengine ya Serikali Kuu, kuwezesha ulipaji kodi kwa hiari na kuchangia maendeleo endelevu ya kijamii na kiuchumi nchini.

Maadhimisho ya miaka 30 ya TRA yanatarajiwa kuwa jukwaa muhimu la kutathmini mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miongo mitatu na kuweka mikakati mipya ya kuimarisha mchango wa kodi katika maendeleo ya Tanzania.






Mke wa Rais wa Singapore, Mheshimiwa Mama Jane Ittogi Shanmugaratnam, ametembelea kituo cha uzalishaji nguo za pamba zinazotengenezwa kwa mikono Msasani jijini Dar es Salaam na kujionea shughuli mbalimbali zinazofanyika katika eneo hilo.

Akiwa katika kituo hicho, Mheshimiwa Mama Jane Ittogi Shanmugaratnam alitembelea maeneo tofauti ya uzalishaji na kushuhudia hatua mbalimbali za uchakataji wa pamba hadi kutengeneza nguo zinazozingatia ubora wa hali ya juu na utunzaji wa mazingira.

Akiwa katika kituo hicho, alielezwa namna wafanyakazi wa kiwanda hicho wanavyotumia ujuzi wa jadi pamoja na teknolojia za kisasa kuzalisha bidhaa za pamba zinazokidhi mahitaji ya masoko ya ndani na kimataifa.

Mhe. Mama Jane alionesha kufurahishwa na ubunifu, ustadi na juhudi zinazofanywa na watumishi wa kiwanda hicho kidogo na wanavyotumia malighafi za ndani na kusisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano wa kimataifa unaolenga kukuza biashara, uwekezaji na maendeleo endelevu.

Rais wa Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam na mwenza wake wako nchini kwa ziara ya siku tatu ya kitaifa ikilenga kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi, biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Singapore.








Na Karama Kenyunko Michuzi Tv

RAIS Samia Suluhu Hassan amesema Tanzania ina fursa kubwa za uwekezaji na iko tayari kuwa lango la Singapore kuingia katika masoko ya Afrika Mashariki, Ukanda wa Maziwa Makuu na Bara la Afrika kupitia Soko Huru la Afrika (AfCFTA).

Akizungumza katika Jukwaa la Biashara na Uwekezaji la Tanzania na Singapore, Rais Samia alisema Tanzania ni moja ya nchi zenye uchumi imara na unaokua kwa kasi barani Afrika, huku ikiwa na nafasi ya kimkakati inayounganisha masoko ya Afrika Mashariki, Kati na Kusini mwa Afrika.

Alisema licha ya mahusiano mazuri ya kidiplomasia kati ya Tanzania na Singapore, bado kuna fursa kubwa ambazo hazijatumika kikamilifu katika biashara na uwekezaji.

Kwa mujibu wa Rais Samia, biashara kati ya nchi hizo iliongezeka kutoka dola za Marekani milioni 74 mwaka 2020 hadi dola milioni 299 mwaka 2023 kabla ya kushuka tena hadi dola milioni 74 mwaka 2024.

Alisema tangu mwaka 1997, Singapore imesajili miradi 36 nchini Tanzania yenye thamani ya dola milioni 535 na iliyozalisha ajira 3,328.

Rais Samia alitaja maeneo yenye fursa kubwa za ushirikiano kuwa ni bandari na usafirishaji, kilimo na usindikaji wa mazao, nishati jadidifu, miundombinu janja, utalii, uchumi wa buluu, huduma za kifedha na utatuzi wa migogoro ya kibiashara.

Alisema Tanzania ni lango la biashara kwa nchi sita zisizo na bandari ambazo ni Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Malawi, Rwanda, Uganda na Zambia, huku Bandari ya Dar es Salaam ikihudumia sehemu kubwa ya biashara hiyo.

Kwa upande wake, Rais wa Singapore, Tharman Shanmugaratnam, alisema Tanzania ni nchi yenye idadi kubwa ya vijana, rasilimali nyingi za asili, fursa zinazoongezeka za uwekezaji na nafasi ya kimkakati inayounganisha masoko ya kikanda na ya kimataifa.

Alisema ushirikiano kati ya Tanzania na Singapore unaweza kuunganisha uzoefu wa Singapore katika usimamizi wa mifumo yenye ufanisi, huduma za thamani ya juu, uchumi wa kidijitali na usimamizi wa minyororo ya ugavi na hivyo kuzalisha ajira, kuongeza ujuzi na kukuza ukuaji jumuishi wa uchumi.

Rais Samia aliwataka wafanyabiashara na taasisi za pande zote mbili kutumia jukwaa hilo kujenga ushirikiano wa kudumu utakaozalisha uwekezaji, biashara na miradi yenye manufaa kwa wananchi wa nchi hizo mbili.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 09 Juni, 2026.
Na Karama Kenyunko Michuzi Tv

TANZANIA na Singapore zimefungua ukurasa mpya wa ushirikiano baada ya kusaini mikataba mitano na hati za makubaliano katika sekta mbalimbali hatua inayolenga kuimarisha biashara, uwekezaji na ushirikiano wa kiuchumi kati ya nchi hizo mbili.

Mikataba iliyosainiwa inahusi kuondoa kodi Mara mbili (Double Taxation) muendelezaji wa ujuzi, biashara za kaboni, mashauriano ya kidiplomasia na uwezeshaji wa biashara.

Mikataba hiyo itapunguza gharama za kufanya biashara, kupunguza vihatarishi vinavyotazamwa na wawekezaji na kuongeza imani kwa wawekezaji wanaotaka kuwekeza katika nchi hizo mbili.

Amesema nchi hizo pia zinaendelea kufanya kazi kuelekea mfumo wa pamoja wa utekelezaji wa biashara ya kaboni chini ya Kifungu cha sita cha Mkataba wa Paris huku zikihamasisha maendeleo endelevu.

Akizungumza katika Jukwaa la Biashara na Uwekezaji la Tanzania na Singapore jijini Dar es Salaam, Rais Tharman amesema dunia inakabiliwa na mazingira mapya ya biashara yenye kutokuwa na uhakika, hivyo kuna umuhimu wa kujenga njia mpya za ushirikiano wa kiuchumi na minyororo imara ya ugavi.

Kwa upande wake, Rais Samia Suluhu Hassan amesema yeye na Rais Tharman walifanya mazungumzo yaliyowezesha kusainiwa kwa makubaliano na hati za ushirikiano kwa manufaa ya nchi hizo mbili.

Amesema hatua hiyo inaonyesha dhamira ya pande zote mbili kuharakisha utekelezaji wa makubaliano yaliyofikiwa na kuinua uhusiano wa Tanzania na Singapore katika viwango vya juu zaidi.

Rais Samia amesema ziara hiyo ya Rais wa Singapore imekuja wakati nchi hizo zikiadhimisha miaka 45 ya uhusiano wa kidiplomasia na kwamba ni mara ya kwanza katika historia Rais wa Singapore kufanya ziara ya kiserikali nchini Tanzania.

Amesema Tanzania na Singapore zinaendelea kufurahia uhusiano mzuri unaojengwa katika misingi ya kuaminiana, ushirikiano na manufaa ya pamoja.

Na hii ni habari ya pili kuhusu fursa za biashara na uwekezaji.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongoza Ujumbe wa Tanzania kwenye mazungumzo na Ujumbe wa Singapore uliongozwa na Rais wa Nchi hiyo Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam, tarehe 09 Juni, 2026.

Viongozi hao wawili wamefanya mazungumzo rasmi yaliolenga kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Singapore katika maeneo mbalimbali hususani biashara, uwekezaji, maendeleo ya rasilimali watu na ujuzi, pamoja na uchumi wa kidijitali.Mazungumzo hayo yalifuatiwa na utiaji saini wa mikataba na Hati za ushirikiano kati ya nchi hizo mbili, na mkutano wa pamoja na waandishi wa habari.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam kwenye mkutano na Waandishi wa Habari uliofanyika, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 09 Juni, 2026.




Top News