Na John Mapepele, Wu hani - China

Serikali ya Tanzania imesisitiza dhamira yake ya kujenga sekta imara ya viwanda vya dawa na kuifanya nchi kuwa kitovu cha uzalishaji wa dawa kwa ukanda wa Afrika Mashariki na kwingineko barani Afrika, huku ikizidi kuvutia uwekezaji wa kimkakati kutoka China.

Akizungumza Julai 7,2026 katika kikao na viongozi wa kampuni ya Jointown Pharmaceutical Group nchini China, inayoongoza kwa uzalishaji wa madawa kwa upande wa makampuni binafsi nchini hapa, Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa amesema Tanzania imejipanga kuendeleza Eneo Maalum la Kiuchumi la Dawa na Vifaa Tiba la Mloganzila, ambalo litakuwa kitovu cha uwekezaji katika uzalishaji wa dawa, malighafi za dawa (APIs) na vifaa tiba.

Amesema, eneo hilo limeboreshwa kwa miundombinu ya kisasa na linaunganishwa kwa urahisi na Bandari ya Dar es Salaam pamoja na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere.

Waziri Mchengerwa amebainisha kuwa Serikali iko tayari kushirikiana na Jointown katika kuanzisha uzalishaji wa malighafi za dawa, hatua itakayoongeza uwezo wa Tanzania kujitosheleza kwa dawa muhimu na kuiwezesha kuhudumia masoko ya kikanda.

“Ushirikiano kati ya Jointown na Bohari ya Dawa (MSD) unatarajiwa kuleta mageuzi katika mifumo ya ugavi, uhifadhi na usambazaji wa dawa nchini kupitia matumizi ya teknolojia na uzoefu wa kampuni hii kubwa hapa China katika usimamizi wa minyororo ya usambazaji duniani” amesema Mhe. Mchengerwa

Aidha Mhe. Mchengerwa amethibitisha Serikali inayoongozwa na Rais wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, inafuatilia kwa karibu uwekezaji wa dawa nchini na ameahidi ushirikiano wa Serikali kwa wawekezaji watakaochangia maendeleo ya sekta ya afya.

Katika kuonesha utayari wa Serikali, Waziri Mchengerwa amesema Tanzania ipo tayari kutenga maeneo ya kutosha kwa ajili ya uwekezaji wa uzalishaji wa malighafi za dawa, akieleza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya dhamira ya dhati ya kuharakisha uanzishwaji wa viwanda vya kisasa vitakavyozalisha dawa kwa matumizi ya ndani na kwa ajili ya soko la Afrika.







Na Mwandishi Wetu
KAMPUNI ya NIC Insurance imewahimiza wamiliki wa vyombo vya moto nchini kuhakikisha wanakata bima ili kujikinga na athari za kifedha zinazoweza kujitokeza pindi yanapotokea majanga au ajali.

Wito huo umetolewa na Afisa Bima wa NIC Insurance, Iman Mollel, wakati akizungumza na waandishi wa habari katika Banda la kampuni hiyo kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere jijini Dar es Salaam.

Mollel amesema NIC Insurance imeendelea kuboresha utoaji wa huduma kwa kuhakikisha madai ya fidia kwa magari yaliyoharibika kiasi cha kutotengenezeka (total loss) yanashughulikiwa kwa haraka, ambapo malipo hufanyika ndani ya siku saba baada ya mteja kukamilisha nyaraka zote zinazohitajika.

Amesema kampuni hiyo inatoa bima kwa aina mbalimbali za vyombo vya moto, ikiwemo magari binafsi, magari ya biashara, magari ya mizigo, mabasi na magari ya abiria, bajaji pamoja na pikipiki, ili kuhakikisha wamiliki wake wanapata kinga dhidi ya hasara zinazoweza kujitokeza.

Aidha, Mollel amesema NIC Insurance imeweka huduma za kidijitali zinazowawezesha wateja kupata huduma za bima kwa njia ya mtandao, hatua inayolenga kupunguza gharama na muda wa kusafiri kufuata huduma katika ofisi za kampuni hiyo.

Ametoa wito kwa wananchi wanaotembelea Maonesho ya Sabasaba kufika katika banda la NIC Insurance ili kupata elimu kuhusu huduma mbalimbali za bima pamoja na ushauri wa kitaalamu utakaowasaidia kuchagua bima zinazokidhi mahitaji yao.






Na Mwandishi Wetu
MAMLAKA ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), kupitia Chuo cha VETA Chang'ombe, imebuni pikipiki ya magurudumu matatu (Bajaj) yenye teknolojia ya kisasa ya kufagia barabara, ubunifu unaolenga kuongeza ufanisi katika usafi wa miji na kupunguza gharama za usafi wa mazingira.

Akizungumza katika Banda la VETA kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere jijini Dar es Salaam, Mwalimu wa Chuo cha VETA Chang'ombe, Emmanuel Bukuku, amesema kifaa hicho kina uwezo wa kufagia barabara urefu wa kilomita mbili kwa saa moja.

Bukuku amesema mashine hiyo imeundwa kwa mfumo unaokusanya vumbi, mchanga na taka ndogondogo wakati wa kufagia na kuzipeleka kwenye sehemu maalumu ya kuhifadhi, hivyo kuacha barabara zikiwa safi na salama kwa matumizi.

Ameeleza kuwa ubunifu huo unaweza kuwa suluhisho kwa halmashauri, manispaa na majiji nchini katika kuboresha huduma za usafi wa barabara kwa kutumia teknolojia ya ndani, badala ya kutegemea nguvu kazi kubwa ya watu pekee.

"Teknolojia hii imeundwa na wataalamu wetu wa VETA kwa kuzingatia mahitaji ya mazingira ya Tanzania. Inaongeza ufanisi, inapunguza muda wa kufanya usafi na inaweza kusaidia kupunguza gharama za uendeshaji wa shughuli za usafi katika mamlaka za serikali za mitaa," amesema Bukuku.

Aidha, amesema Chuo cha VETA Chang'ombe kipo tayari kupokea maombi kutoka kwa taasisi za umma na binafsi kwa ajili ya kutengeneza vifaa hivyo kulingana na idadi na mahitaji ya mteja, hatua inayolenga kuendeleza matumizi ya teknolojia za ubunifu zinazotengenezwa nchini.
Mkutano Mkuu wa Kwanza wa Baraza la Mawaziri wa Masuala ya Kijamii wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) umehitimishwa Julai 7, 2026 jijini Dar es Salaam, kwa kusainiwa kwa ripoti maalumu inayohusu uwekaji wa sera na mikakati thabiti katika sekta za jinsia, watoto, vijana, wazee, hifadhi ya jamii, kazi, ajira na uhamiaji.

Mawaziri kutoka nchi zote 8 wanachama wa EAC wameidhinisha na kusaini ripoti hiyo ili ianze kutekelezwa kikanda, ikilenga kuhakikisha kuwa faida za mtangamano wa kiuchumi na kijamii zinamfikia kila mwananchi kwa usawa, baada ya kupitia mapendekezo yaliyowasilishwa na wataalamu na Makatibu Wakuu.

Mkutano huo wa kihistoria uliongozwa na Naibu Waziri Mkuu wa Kwanza na Waziri anayeshughulikia Ushirikiano wa Afrika Mashariki wa Uganda, Mhe. Rebecca Kadaga, ambaye aliongoza zoezi la utiaji saini wa ripoti hiyo kwa kushirikiana na Mawaziri wenzake wa ukanda huo.

Ujumbe wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika mkutano huo uliongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Maendeleo ya Vijana) Mhe. Joel Nanauka, akiambatana na Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu, Mhe. Maryprisca Mahundi, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Mhe. Dkt. Eveline Munisi, pamoja na Makatibu Wakuu, wataalam wa wizara husika, na wa mifuko ya hifadhi ya jamii nchini.

Katika majadiliano hayo, viongozi hao walisisitiza kuwa utekelezaji wa sera hizi utaleta mageuzi makubwa na ya kihistoria katika mifumo ya ajira, ulinzi wa jamii, ustawi wa makundi maalum, pamoja na usimamizi madhubuti wa masuala ya uhamiaji katika ukanda mzima.

Kuhitimishwa kwa mkutano huo na kusainiwa kwa ripoti hii ya pamoja kunadhihirisha dhamira thabiti ya EAC katika kujenga ukanda wenye sera shirikishi, maendeleo jumuishi, na ustawi endelevu kwa wananchi wake.












Na Mwandishi Wetu
MAMLAKA ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) imewahimiza Watanzania kushiriki kikamilifu katika mapambano dhidi ya dawa duni na zisizo salama, ikisisitiza kuwa ulinzi wa afya ya jamii ni jukumu la kila mwananchi.

Hayo ameyasema Meneja wa Mawasiliano na Elimu kwa Umma wa TMDA, Gaudensia Simwanza, alipokuwa akitoa elimu kwa wananchi waliotembelea banda la TMDA katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere jijini Dar es Salaam.

Simwanza amesema dawa duni na zisizosajiliwa mara nyingi huingizwa nchini kwa njia zisizo rasmi, hivyo wananchi wanapaswa kuwa macho na kutoa taarifa mara wanapobaini bidhaa zinazotiliwa shaka badala ya kuzifumbia macho.

Ameeleza kuwa matumizi ya dawa duni yanaweza kusababisha madhara makubwa kwa afya ya watumiaji na kuhatarisha maisha ya wananchi, jambo linaloweza kuathiri nguvu kazi na maendeleo ya taifa.

Aidha, amewataka wananchi kujenga utamaduni wa kukagua tarehe za mwisho wa matumizi wa dawa kabla ya kuzinunua au kuzitumia. Amesema endapo watabaini dawa zilizokwisha muda wake wa matumizi au zinazoshukiwa kuwa duni, wanapaswa kutoa taarifa TMDA ili zichukuliwe hatua za kuziondoa sokoni.

Gaudensia amesisitiza kuwa dawa duni hazina nafasi katika soko la Tanzania, akibainisha kuwa mafanikio ya kuzuia bidhaa hizo yanategemea ushirikiano wa karibu kati ya TMDA na wananchi katika kulinda afya ya jamii.

📍 Aielekeza kuboresha mikakati ya kudhibiti migongano kati ya wanyamapori na binadamu

Na Beatus Maganja, Morogoro

Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb.) ameipongeza Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) kwa mafanikio yake katika kuvutia wawekezaji jambo lililotajwa kuchangia ongezeko la mapato ya Taasisi hiyo, huku akiielekeza Menejimenti ya mamlaka hiyo kuandaa mikakati ya muda mfupi, ya kati na ya muda mrefu ya kudhibiti migongano baina ya wanyamapori na binadamu.

Akizungumza na Bodi ya Wakurugenzi na Menejimenti ya TAWA alipofanya ziara ya kikazi katika Ofisi za Makao Makuu ya TAWA mkoani Morogoro Julai 7, 2026, Dkt. Kijaji alisema mwaka mpya wa fedha unapaswa kuwa mwanzo wa utekelezaji wenye matokeo makubwa katika kuimarisha uhifadhi wa maliasili na kuongeza kasi ya kudhibiti migongano kati ya binadamu na wanyamapori ili kuhakikisha usalama wa wananchi na wanyamapori kwa pamoja.

"Tunapaswa kuwa na mikakati ya muda mfupi, wa kati na mrefu itakayowezesha kupunguza migongano kati ya wanyamapori na binadamu. Lengo letu ni kuona wananchi wanakuwa salama na wanyamapori wanaendelea kuhifadhiwa" alisema Dkt. Kijaji.

Aidha, Waziri huyo aliielekeza TAWA kuendelea kuimarisha ushirikiano na wananchi wanaozunguka maeneo ya hifadhi, akisisitiza kuwa wananchi ndiyo walinzi namba moja wa rasilimali za wanyamapori. Pia alisisitiza kuimarishwa kwa ulinzi wa maeneo ya hifadhi kwa kutoruhusu shughuli za kibinadamu ndani ya maeneo hayo, ikiwemo uvamizi kwa ajili ya kilimo na matumizi mengine yasiyoruhusiwa kisheria.

 Vilevile Mheshimiwa Waziri Kijaji aliipongeza TAWA kwa usimamizi mzuri wa fedha za Serikali hususan katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo pamoja na matumizi ya teknolojia katika shughuli mbalimbali za uhifadhi.

Awali akiwasilisha taarifa ya utendaji wa Bodi ya Wakurugenzi wa TAWA, Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Mej. Jen. (Mstaafu) Hamis R. Semfuko, alisema kuimarika kwa ulinzi na usimamizi wa rasilimali za wanyamapori kumechangia ongezeko la idadi ya wanyamapori katika maeneo yanayosimamiwa na mamlaka hiyo. Alisema kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2025, idadi ya swala aina ya Puku imeongezeka kutoka 1,950 mwaka 2021 hadi 3,185 mwaka 2025, sawa na ongezeko la asilimia 63. Aidha, kaya 1,107 zilizokuwa katika Kijiji cha Ngombo, Wilaya ya Malinyi zimehama kutoka ndani ya Pori la Akiba Kilombero kufuatia utatuzi wa migogoro ya matumizi ya ardhi.

Semfuko alisema TAWA pia imeendelea kuimarisha uwekezaji baada ya kusaini mikataba mitatu ya uwekezaji mahiri na kufikisha jumla ya maeneo 16 ya uwekezaji huo, ambao kwa sasa unachangia asilimia 46 ya mapato ya mamlaka. Vilevile, idadi ya watalii wa picha imeongezeka na kufikia 267,575 ikilinganishwa na watalii 240,967 waliotembelea maeneo yanayosimamiwa na TAWA katika mwaka wa fedha 2024/25.

Aliongeza kuwa TAWA imeimarisha mwitikio wa matukio ya wanyamapori wakali na waharibifu kwa kukamilisha ujenzi wa mabwawa 14, vizimba 31 na vituo 14 vya askari, hatua iliyochangia kuokoa maisha ya wananchi na mali zao.

 Aidha, gawio la shilingi bilioni 9.7 limetolewa kwa WMA 16, vijiji 161 na Halmashauri za Wilaya 41, huku maelfu ya wananchi wakiendelea kunufaika na shughuli za uvuvi na ufugaji nyuki katika maeneo ya hifadhi. Kwa upande wa utendaji wa taasisi, alisema TAWA pia imeajiri watumishi 661 kuongeza nguvu kazi na kufikia makusanyo ya shilingi bilioni 92.28 hadi Juni 2026, ikilinganishwa na shilingi bilioni 87.32 zilizokusanywa mwaka uliotangulia.

Katika ziara hiyo, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb.) aliambatana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi, pamoja na Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Wizara, Bw. Bernard Marcelline. Ziara hiyo imeendelea kudhihirisha dhamira ya Serikali ya kuimarisha usimamizi wa rasilimali za wanyamapori ili kuleta manufaa kwa wananchi, sambamba na kutafuta mwarobaini wa kukabiliana na changamoto za migongano baina ya wanyamapori na binadamu.









NA MWANDISHI WETU, AFRIKA KUSINI

Waziri wa Maji, Jumaa Aweso pamoja na ugeni wake, wapo nchini Afrika Kusini, ikiwa ni ziara ya kikazi yenye lengo la kushirikiana na wadau mbalimbali katika kufanikisha udhibiti wa upotevu wa maji ili kuongeza kasi ya usambazaji wa huduma ya maji kwa wananchi.

Ziara hiyo iliyoanza Julai 6, 2026, imelenga kushiriki kikao kazi na wataalamu wa masuala ya teknolojia zenye uwezo wa kudhibiti upotevu wa maji, ili wananchi waweze kupata maji safi, salama na yenye kutosheleza kwa matumizi mbalimbali ya kijamii na kiuchumi.

Ikumbukwe kuwa, upotevu wa maji ni miongoni mwa changamoto inayoikabili Wizara ya Maji, ambayo imesababisha kupotea kwa maji mengi na kuzikosesha mapato mamlaka za maji katika wilaya mbalimbali nchini.

Kimsingi, moja ya kipaumbele cha Wizara ya Maji kwa mwaka wa fedha 2026/2027 ni kupambana na upotevu wa maji. Hivyo ziara hiyo, ni mkakati wa kufanikisha kipaumbele hicho.

Katika ziara hiyo, Aweso ameambatana na Katibu Mkuu wa Wizara, Mhandisi Mwajuma Waziri, Balozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini, James Bwana pamoja na wataalamu wengine wa wizara hiyo.

Pamoja na masuala ya maji, Julai 7, akiwa nchini humo, Aweso pamoja na ugeni wake wameshiriki kikamilifu hafla ya maadhimisho ya Siku ya Kiswahili Duniani.

Katika hafla hiyo, amezindua Kituo cha Utamaduni wa Kiswahili Tanzania (Tanzania Kiswahili Cultural Center) ikiwa ni mkakati wa kufundisha lugha ya Kiswahili kwa wageni ili kuendelea kukuza lugha hiyo na utamaduni wa Kitanzania ulimwenguni.










KAMANDAwa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam Jumanne Muliro ameridhishwa na ushirikishwaji wa vijana katika uendelezaji wa miradi ya gesi asilia inayoendelea mkoani Mtwara.

Akizungumza katika banda la Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) kwenye maonesho ya Sabasaba Kamanda Muliro amesema ni vema miradi hiyo ikaendelea kushirikisha vijana kwani serikali inaendelea kutoa hamasa kwa vijana kujikita katika sekta ndogo ya mafuta na gesi.

Kwa upande wake Mjiolojia kutoka PURA Lukelo Matimbwi amemueleza Kamanda Muliro kuwa katika mradi wa uzalishaji wa gesi asilia unaoendelea Mnazi Bay zaidi ya asilimia 90 wanaofanya kazi hapo ni vijana wa kitanzania.

Ameongeza kuwa katika mradi wa uzalishaji wa gesi asilia Songo Songo pia ushirikishwaji wa vijana wa kitanzania ni mkubwa sana katika utekelezaji wa mradi huo.

Kamanda Muliro ametembelea banda la PURA kwenye Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara maarufu kama Sabasaba.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga (Mbinga DC) Joseph Rwiza Kashushura, pamoja na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Mbinga (Mbinga TC), Amina H. Seif, wametembelea Banda la Mkoa wa Ruvuma katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), Julai 7, 2026.

Katika maonesho hayo, wajasiriamali kutoka Mkoa wa Ruvuma ni miongoni mwa washiriki waliopata nafasi ya kuonesha bidhaa na huduma zao, hatua inayowapa fursa muhimu ya kutangaza biashara zao, kupata masoko ya uhakika, kuunganisha mitandao ya kibiashara na kujifunza mbinu mbalimbali kutoka kwa wajasiriamali wengine wanaoshiriki maonesho hayo.

Maonesho ya 50 ya Sabasaba yanaendelea kuwa jukwaa muhimu la kukuza biashara, uwekezaji na ubunifu kwa kuwaunganisha wazalishaji, wajasiriamali, wawekezaji na wadau mbalimbali wa maendeleo ya uchumi kutoka ndani na nje ya Tanzania.









Na.Ashura Mohamed -Arusha


‎‎Wadau wa sekta ya kilimo, biashara, mazingira na teknolojia kutoka ndani na nje ya Afrika wanatarajiwa kukutana jijini Arusha katika Mkutano wa Kwanza wa Uchavushaji Afrika, unaolenga kuweka mkakati wa pamoja wa kulinda wachavushaji na kuimarisha kilimo endelevu barani Afrika.

‎Mkutano huo unatarajiwa kufanyika kuanzia Septemba 29 hadi Oktoba 1, 2026, ukiandaliwa na Shirika la Maendeleo Endelevu ya Kilimo na Biashara za Kilimo Tanzania (SAADIT) kwa kushirikiana na taasisi mbalimbali, ikiwemo Green Rural Community and workers bees Africa huku ukipata utambuzi rasmi kutoka Wizara ya Viwanda na Biashara.

‎Kupitia mkutano huo, wadau watajadili changamoto na fursa zinazohusu uchavushaji, pamoja na namna ya kuingiza uhifadhi wa wachavushaji katika sera na mipango ya maendeleo ili kuongeza uzalishaji wa mazao, kuimarisha usalama wa chakula na kukuza uchumi wa kilimo.

‎Mkurugenzi na Mwanzilishi wa SAADIT, Malulu Martin Igobeko, amesema kupungua kwa idadi ya wachavushaji kutokana na uharibifu wa mazingira na matumizi yasiyo sahihi ya viuatilifu ni tishio kwa mifumo ya uzalishaji wa chakula barani Afrika.

‎Amesema mkutano huo utakuwa jukwaa la kuunganisha serikali, sekta binafsi na washirika wa maendeleo katika kutafuta suluhisho la changamoto hiyo na kuhakikisha huduma za uchavushaji zinalindwa kwa maendeleo ya kilimo.

‎“Wachavushaji wanapungua kwa kasi kutokana na uharibifu wa maeneo wanayoishi na matumizi yasiyo sahihi ya viuatilifu. Bila wao, uzalishaji wa mazao na usalama wa chakula unaweza kuathirika,” amesema Igobeko.

‎Kwa upande wake, Genya Charles kutoka Wizara ya Viwanda na Biashara, amesema uchavushaji unapaswa kuonekana kama sehemu muhimu ya uchumi wa kijani na biashara, kutokana na mchango wake katika kuongeza thamani ya mazao na kufungua fursa za uwekezaji.

‎Naye Mercy Butta kutoka Idara ya Usalama wa Chakula katika Wizara ya Kilimo, amesema mchango wa nyuki na wachavushaji wengine ni muhimu katika kuongeza uzalishaji wa mazao na kuimarisha upatikanaji wa chakula nchini.

‎Katika mkutano huo, kampuni ya teknolojia ya ufugaji nyuki kutoka Australia, BeeSTAR Technology, inatarajiwa kuonyesha teknolojia za kisasa ikiwemo mizinga janja, matumizi ya akili bandia na mifumo ya kidijitali ya kufuatilia uzalishaji wa nyuki.

‎Teknolojia hizo zinatarajiwa kusaidia kuongeza uzalishaji wa asali, kupunguza upotevu wa mizinga na kuboresha huduma za uchavushaji katika sekta ya kilimo.

‎Aidha, mkutano huo utaangazia mpango wa kuongeza mizinga milioni moja unaolenga kuimarisha huduma za uchavushaji katika maeneo ya kilimo kupitia ushirikiano wa wadau mbalimbali.

‎Washiriki wa mkutano huo wakiwemo Green Rural Community and workers bees Africa, Innovative Community Solutions ( ICS), wanatarajiwa kujadili masuala ya utafiti, teknolojia, sera, uwekezaji na mikakati ya maendeleo kwa kushirikisha taasisi mbalimbali za kitaifa na kimataifa.






WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema kuna haja ya kutafuta mbinu mpya ya kukieneza Kiswahili baada ya kuwa kimepata hadhi ya kimataifa.

“Kadiri Kiswahili kinavyoendelea kupata hadhi ya kimataifa, ni muhimu sasa kuanza kutazama hatua inayofuata ya kukieneza duniani. Mataifa mengi yamefanikiwa kueneza lugha na utamaduni wao kupitia vituo vya utamaduni vilivyoanzishwa katika nchi mbalimbali duniani,” amesema.

Ametoa wito huo leo (Jumanne, Julai 7, 2026) wakati akizungumza na washiriki waliohudhuria kilele cha Maadhimisho ya Tano ya Siku ya Kiswahili Duniani kwenye ukumbi wa mikutano wa ofisi za makao makuu ya UNESCO jijini Paris, Ufaransa.

“Serikali itaendelea kuimarisha matumizi ya Kiswahili ndani na nje ya nchi kupitia elimu, tafiti, uchapishaji, tafsiri, teknolojia za kidijiti na diplomasia ya lugha. Tutaendelea kushirikiana na UNESCO, nchi mbalimbali, vyuo vikuu, taasisi za kimataifa na wadau mbalimbali katika kuendeleza lugha hii kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho,” amesema.

Waziri Mkuu ambaye alikuwa mgeni rasmi kwa niaba ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema sasa hivi Kiswahili kimeshatambulika kuwa lugha rasmi ya EAC na SADC. “Kiswahili ndiyo utambulisho wetu wana jumuiya ya Afrika Mashariki. Mtu akiongea Kiswahili anajulikana kuwa anatokea Tanzania, Burundi, Congo au Sudan Kusini. Na pia kimekuwa moja ya lugha rasmi za Umoja wa Afrika (AU),” amesema.

“Si hivyo tu, sasa hivi Kiswahili kinatambulika kuwa ni lugha rasmi ya mikutano mikubwa ya UNESCO kutokana na pendekezo lililopitishwa kwa kaulimoja Novemba, 2025 wakati wa Mkutano Mkuu wa 43 wa UNESCO, uliofanyika Samarkand, Uzbekistan.”

Amesema kwa mujibu wa wataalamu wa lugha, Kiswahili kinazungumzwa na watu kati ya milioni 300 hadi milioni 500 na idadi hiyo inaendelea kuongezeka kutokana na matumizi yake katika elimu, biashara, vyombo vya habari, teknolojia ya habari na mawasiliano pamoja na mitandao ya kijamii.

“Hali hiyo inaonesha kwamba Kiswahili siyo mali ya Watanzania pekee bali ni urithi wa Afrika na zawadi ya Afrika na dunia. Kiswahili kinaunganisha watu, Kiswahili kinaunganisha biashara, Kiswahili kinaunganisha jamii,” amesisitiza.

Mapema, Mkurugenzi Mkuu wa UNESCO, Prof. Khaled El-Enany aliwaeleza washiriki wa maadhimisho hayo kwamba shirika lake limesaidia kufadhili uandaaji wa kamusi ya Kifaransa kwenda Kiswahili.

“Mbali na matumizi ya kawaida kwa watalii au watu wanaojifunza lugha, tunatarajia kwamba uwepo wa kamusi hiyo na nyaraka nyingine kutasaidia kuongeza fursa kwa walimu na wanafunzi wanaojifunza Kifaransa na Kiswahili,” amesema.

Amesema uzuri wa Kiswahili ni lugha ambayo imekuwa ikiendelea kukua na kuvuka mipaka bila kupoteza uasili wake na imeunganisha watu bila kulazimika kuvuka mipaka ya nchi zao.

Akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na washiriki hao, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda alisema Tanzania ina lugha za makabila zaidi ya 150 katika maeneo mbalimbali lakini wananchi wake wameweza kuunganishwa na lugha moja ya Kiswahili.

Alisema wakati jijini Paris, Ufaransa wakiadhimisha kilele cha maadhimisho hayo na kongamano la pili lililoandaliwa na UNESCO kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania, nchi nyingine tatu za Uingereza, Algeria na Burundi nazo pia leo zimeadhimisha makongamano kama hayo.

Awali, Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa, Bw. Saidi Othman Yakub alisema maadhimisho hayo ya tano ambayo yanafanyika sambamba na Kongamano la Pili la Siku ya Kiswahili Duniani, yamevutia washiriki zaidi ya 300 kutoka nchi 16 duniani.

Amezitaja nchi hizo kuwa ni Comoro, Tanzania, Ujerumani, Marekani, Canada, Uingereza, Italia, Luxembourg, Sweden, Ubelgiji, Austria, Uturuki, Misri, Kenya, Uganda na wengi kutoka Tanzania.

“Tangu tarehe 4 Julai hadi leo tarehe 7 Julai, 2026 tumeshuhudia shughuli mbalimbali zilizolenga kuendeleza na kukitangaza Kiswahili duniani. Shughuli hizo zilijumuisha matembezi ya hamasa katika mitaa maarufu ya Jiji la Paris, hafla za vyakula vya Kiswahili kwa Diaspora, kongamano kuhusu nafasi ya Kiswahili katika biashara na uchumi, semina na warsha mbalimbali hapa UNESCO.

Amesema waliandaa pia tamasha la Usiku wa Mswahili lililofanyika chini ya Mnara wa Eiffel kandokando ya Mto Seine, maonesho ya filamu na chakula pamoja na kazi za Kiswahili.


































Top News