Na Janeth Raphael MichuziTv

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amezindua rasmi Jengo la Tiba ya Mionzi kwa Wagonjwa wa Saratani katika Kilimanjaro Christian Medical Centre (KCMC), hatua inayotarajiwa kuimarisha huduma za matibabu ya saratani na kupanua upatikanaji wa huduma za kibingwa nchini.

Uzinduzi huo uliofanyika katika hospitali hiyo iliyopo Moshi, Mkoani Kilimanjaro umeelezwa kuwa sehemu ya jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita za kuboresha sekta ya afya kwa kuwekeza katika miundombinu ya kisasa ya matibabu na teknolojia za huduma za kibingwa.

Jengo hilo jipya la tiba ya mionzi linatarajiwa kuongeza uwezo wa KCMC kutoa huduma za kisasa za uchunguzi na matibabu ya saratani, huku likipunguza changamoto ya wagonjwa kusafiri umbali mrefu kufuata huduma hizo katika maeneo mengine ya nchi.

Akizungumza katika hafla hiyo, Rais Samia amesisitiza dhamira ya serikali ya kuendelea kuboresha huduma za afya kwa wananchi kupitia uwekezaji katika vifaa tiba, miundombinu na rasilimali watu, ili kuhakikisha huduma bora zinapatikana karibu na wananchi.

Kukamilika kwa mradi huo kunatajwa kuwa hatua muhimu katika kuimarisha mapambano dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza, hususan saratani, ambayo imeendelea kuwa miongoni mwa changamoto kubwa za afya nchini.

Kwa kuanza kutumika kwa kituo hicho, wagonjwa kutoka Kanda ya Kaskazini na maeneo jirani wanatarajiwa kunufaika na huduma za tiba ya mionzi kwa urahisi zaidi, jambo litakalosaidia kuharakisha upatikanaji wa matibabu na kuongeza matumaini ya uponaji kwa wagonjwa wengi.






Kijana Joseph Mtei mwenye mahitaji maalum ambaye kwa sasa anafanya kazi katika kampuni tangu ya UJUZI katika  kiwanda cha kutengeneza samani cha VETA Dodoma, amepongeza uamuzi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa kumuwezesha kupata ajira rasmi.

Agizo hilo lilitolewa Juni 23, 2026, wakati wa kilele cha wiki ya utumishi wa umma Jijini Dodoma na Waziri wa TAMISEMI, Profesa Riziki Shemdoe, ambaye alimwelekeza Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala bora, kuhakikisha Joseph Mtei anapatiwa ajira rasmi, amesema hatua hiyo imeonyesha kuwa serikali inatambua uwezo wa watu wenye ulemavu na kuthamini mchango wao katika maendeleo ya taifa.

Akizungumza katika mahojiano maalum na Michuzi TV Juni 24, 2026, jijini Dodoma, Mtei alisema safari yake ya maisha imekuwa ya changamoto nyingi tangu utotoni na licha ya kuzaliwa bila mikono lakini hakukata tamaa, Ameeleza kuwa elimu na mafunzo ya ufundi vimemwezesha kujijengea uwezo wa kufanya kazi na kujitegemea kama ilivyo kwa watu wengine wasiokuwa na ulemavu.

Joseph amesema fursa hiyo inapaswa kuwa chachu kwa vijana wengine wenye mahitaji maalum kuendelea kupambana na changamoto zinazowakabili na kutumia fursa zilizopo kujiletea maendeleo, ameeleza kuwa mafanikio yake ni matokeo ya juhudi binafsi, msaada alioupata kwa baadhi ya wadau waliomsapoti kupata elimu pamoja na mazingira yaliyomruhusu kuonyesha uwezo wake kazini.

Aidha, ametoa wito kwa wazazi na jamii kuacha kuwaficha watoto wenye ulemavu na badala yake kuwapa nafasi ya kusoma, kujifunza na kushiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii na kiuchumi, amesema kwa sasa anaishi maisha ya kujitegemea, analipa kodi, anamsomesha mdogo wake, jambo linalothibitisha kuwa ulemavu si kikwazo cha mafanikio.




Na Victor Masangu, Pwani


Serikali ya awamu ya sita katika kupambana na changamoto ya ukosefu wa ajira imeamua kuja na mpango kabambe wa kuanzisha shindano linalojulikana kwa jina la Vijana uchumi Challenge lenye lengo la kuwakutanisha vijana mbali mbali ili waweze kutoa kutoa mawazo yenye kuleta tija katika kuisaidia serikali katika nyanja mbali mbali ikiwemo uchumi na maendeleo.

Hayo yamebainishwa na Naibu Katibu Ofisi ya Rais maendeleo ya vijana Dkt. Kedmon Mapana wakati wa halfa ya uzinduzi rasmi wa kambi maalumu kwa ajili ya usahili wa vijana wapatao 100 bora ambao wamepata fursa ya kuchaguliwa kati ya vijana elfu 7852 walioshiriki hapo awali kutoka mikoa mbali mbali ipatayo 27 ya Tanzania bara na visiwani.

Pia amebainisha kwamba ana imani vijana hao 100 ambao wamechaguliwa na kuweka kambi wataweza kuleta matokeo chanya na kwamba serikali itaendelea kushirikiana nao bega kwa bega na kuchukua mawazo yao ambayo watakwenda kuyafanyia kazi na kuyaendeleza katika maeneo mbali mbali.

"Sisi kama serikali tumeona ni muhimu sana kuwashirikisha vijana wetu wa Tanzania ambao ndio Taifa letu la kesho katika shindano hili ili waweze na wao kuchangia mawazo yao mbali mbali ambayo yataweza kuketa tija zaidi katika kuisaidia serikali katika nyanja mbali mbali za kiuchumi na mambo mengine ya kimaendeleo na mimi nashukuiru sana vijana hao 100 kwa kujitokeza kwa wingi,"amesema Naibu Katibu huyo.

Kadhalika amesema kwamba baada ya kambi hiyo ya vijana watachaguliwa kutoka 100 hadi kufikia vijana 10 ambao watakwenda katika shindano la fainali litakalofanyika mwezi ujao tarehe 6 na kwamba mshindi wa kwamba atajinyakulia shilingi milioni 50, mshindi wa pili milioni 30 na mshindi wa tatu milioni 20 na wengine waliobaki watapewa kifuta jasho.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa kamati ya Kitaifa ya shindano hilo la vijana Uchumi Challenge Joseph Malekele amesema kwamba washirki hao wataweka kambi kwa kipindi cha muda wa siku nne katika katika shule ya Uongozi Mwalimu Julias Nyerere iliyopo Wilaya ya Kibaha Mkoa wa Pwani ambapo pia watapatiwa mafunzo kutoka kwa jopo la majaji mbali mbali.

Mwenyekiti huyo amesema kwamba lengo kubwa la kuandaa shindano hilo ni kuweza kupata mawazo bunifu kutoka kwa vijana ambayo yanaweza kutekelezeka na kuchangia kwa kiasi kikubwa masuala mazima ya kukuza uchumi pamoja na kuweka misingi endelevu katika maendeleo katika sekta mbali mbali za kilimo, usafirishaji, biashara na mambo mengineyo.

Nao baadhi wa vijana hao ambao wamepata fursa ya kuingia katika kambi hiyo akiwemo Raiani Amour na Adrian Thomas wamebainisha kwamba wana imani mawazo na ubunifu wao utaweza kwenda kuleta matokeo chanyaa katika kuwasaidia vijana hasa ambao wamekuwa na changamoto katika ukosefu wa ajira.

Aidha wameipongeza kwa dhati serikali ya awamu ya sita kwa kushirikiana na Wizara ya vijana kwa kuweza kuona umuhimu mkubwa wa kuwakutanisha vijana kutoka maeneo mbali mbali kwa ajili ya kutoa mawazo yao mbali mbali ili kuweza kuisaidia serikali katika mambo mbali mbali.

Kilele cha Shindano hilo la Vijana Challenge kwa mwaka wa 2026 linatarajiwa kufanyika tarehe 6 ya mwezi ujao Jijini Dar es Salaam ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Rais Dkt, Samia Suluhu Hassan.








NA MWANDISHI WETU, DODOMA

Wanawake, vijana na wenye mahitaji maalum sasa wamefikiwa na bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027, kufuatia bajeti hiyo kuongeza asilimia za mikopo ya makundi hayo kutoka asilimia kumi hadi 15.

Akizungumzia suala hilo, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa na Mbunge wa Viti Maalum wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mary Chatanda, Juni 23, 2026, Jijini Dodoma, amesema Rais Dk. Samia Suluhu Hassan anayajali makundi hayo kwa maneno na kwa matendo, ndiyo maana ameamua kuongeza asilimia za mikopo yao.

"Uwezeshaji wananchi kiuchumi hasa makundi ya wanawake, vijana na wenye mahitaji maalum ni miongoni mwa vipaumbele vya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, ameona asilimia kumi haitoshi, ameongeza asilimia tano zaidi ili kuhakikisha makundi hayo yananufaika na fursa za kiuchumi kwa ustawi wao," amesema Chatanda.

Sambamba na hilo, Chatanda amesema katika mipango ya maendeleo ni vyema kuhakikisha makundi yote yanajumuishwa ili maendeleo tarajiwa yaweze kugusa watu wote kwani hayo ndiyo maendeleo lenye tija kwa Taifa.

"Tanzania tunajenga uchumi shindani na jumuishi, kwa kuhakikisha hilo linafikiwa, ndiyo maana makundi haya yanapewa kipaumbele kwani mafanikio yao yana mchango katika ujenzi wa uchumi wa Taifa zima," amesema.

Kadhalika, Chatanda amesisitiza makundi hayo wapewe mafunzo ya kutosha ya kiujasiriamali ili waweze kutumia vyema mikopo hiyo katika kujiletea maendeleo.

"Maofisa wetu wa maendeleo ya jamii ngazi za kata na wilaya kwa kushirikiana na taasisi za fedha kama mabenki, watoe mafunzo ya namna bora ya kufanya biashara na shughuli nyingine za kiuchumi, ili waweze kuwa na uwezo wa kurejesha mikopo hiyo," amesisitiza.

Katika mabadiliko chanya yaliyofanyika katika bajeti ya mwaka 2026/2027, ni kuongeza asilimia za mikopo kutoka kumi hadi 15 ili kuwezesha makundi hayo kunufaika zaidi kiuchumi likiwepo suala la uboreshaji wa mazingira ya kufanyia shughuli zao za kiuchumi. 



Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma 

Serikali imechukua Hatua Kudhibiti Migogoro ya Wakulima na Wafugaji Mto Lukuledi Ndanda

Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI imesema inatambua changamoto ya uvamizi wa wafugaji katika maeneo ya wakulima katika ushoroba wa Mto Lukuledi, Jimbo la Ndanda, hususan wakati wa ukame ambapo migogoro ya matumizi ya ardhi huongezeka.

Akijibu swali bungeni leo Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI) Dkt  Jafar Seif ameeleza kuwa Serikali kwa kushirikiana na Mamlaka za Serikali za Mitaa pamoja na vyombo vya ulinzi na usalama imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kudhibiti hali hiyo ili kuhakikisha amani na utulivu vinadumishwa kati ya wakulima na wafugaji.

Serikali imeeleza kuwa moja ya hatua kubwa zilizochukuliwa ni pamoja na kupima na kutenga maeneo maalum ya malisho yenye ukubwa wa takribani hekta 129,489.48 katika vijiji 30 vya Mkoa wa Lindi, ikiwemo vijiji vilivyo karibu na bonde la Mto Lukuledi, Ndanda. Hatua hii inalenga kupunguza msongamano wa mifugo katika maeneo ya kilimo na kuzuia migogoro inayojitokeza mara kwa mara.

Aidha, Serikali inaendelea kutoa elimu kwa wafugaji kuhusu umuhimu wa kuachana na ufugaji wa kuhamahama na badala yake kuelekea katika ufugaji wa kisasa unaozingatia tija na biashara. Elimu hiyo inalenga pia kubadilisha mtazamo kuhusu matumizi bora ya ardhi na uhifadhi wa mazingira.

Serikali imetoa wito kwa wafugaji kote nchini kuhakikisha wanazingatia mipango ya matumizi bora ya ardhi pamoja na kutumia kikamilifu maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya malisho kwa kuyaendeleza kupitia kuondoa vichaka na kupanda malisho yanayoendana na ikolojia ya maeneo husika.

Kwa mujibu wa Serikali, utekelezaji wa mikakati hiyo utasaidia kuhakikisha upatikanaji wa malisho ya kutosha mwaka mzima, kupunguza migogoro ya mara kwa mara kati ya wakulima na wafugaji, na hatimaye kuimarisha amani na maendeleo endelevu katika maeneo ya vijijini.



NA DENIS MLOWE IRINGA


ZAIDI ya vijana 200 kutoka vijiji 61 vinavyozunguka Shamba la Miti la Taifa la Sao Hill wilayani Mufindi, mkoani Iringa, wamehitimu mafunzo maalumu ya kukabiliana na majanga ya moto wa misitu ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha ulinzi wa rasilimali za misitu na mazingira kwa ujumla.

Mafunzo hayo yametolewa baada ya kufanyika mchakato wa usaili uliowahusisha zaidi ya vijana 400 waliojitokeza kupima utimamu wa mwili na akili kwa lengo la kushiriki katika kikosi cha kukabiliana na moto wa misitu hatua hiyo imeelezwa kuwa ni mkakati wa kuhakikisha kunakuwa na nguvu kazi ya kutosha yenye uelewa wa masuala ya usalama wa misitu katika maeneo yanayozunguka shamba hilo kubwa la miti.

Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Msaidizi wa Mhifadhi Mkuu wa Shamba la Miti la Taifa la Sao Hill, PCO Said Singano, alisema ushirikishwaji wa vijana kutoka vijiji vinavyozunguka shamba hilo ni njia bora ya kujenga uelewa wa pamoja kuhusu umuhimu wa kulinda misitu na kuzuia hasara zinazoweza kusababishwa na moto.

Alisema moto wa misitu umekuwa tishio kubwa katika maeneo mbalimbali ya misitu nchini, hivyo ni muhimu kuendelea kutoa elimu na mafunzo kwa wananchi wanaoishi karibu na maeneo hayo ili wawe sehemu ya suluhisho la changamoto hiyo.
Aliongeza kuwa vijana waliopatiwa mafunzo wamefundishwa mbinu mbalimbali za kutambua vihatarishi vya moto, namna ya kuzuia kuenea kwa moto pamoja na hatua za haraka za kuchukua pindi moto unapozuka.

Singano alisema kuwa ushiriki wa wananchi katika shughuli za uhifadhi umeendelea kuleta matokeo chanya kwa kuwa jamii imekuwa na uelewa mkubwa zaidi kuhusu thamani ya misitu katika maendeleo ya kiuchumi na uhifadhi wa mazingira.

Alibainisha kuwa Shamba la Miti la Taifa la Sao Hill linaendelea kushirikiana na vijiji vinavyolizunguka ili kuhakikisha misitu inalindwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Kwa upande wake, Afisa wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Wilaya ya Mufindi, Sajenti Guntramu Mlenge, alisema ushirikiano uliopo kati ya Jeshi la Zimamoto na Uokoaji pamoja na Shamba la Miti la Sao Hill umechangia kwa kiasi kikubwa kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu namna ya kujikinga na majanga ya moto.

Alisema kupitia mafunzo hayo, vijana wamepata maarifa ya kutumia vifaa vya kuzimia moto, kutengeneza njia za kuzuia moto kuenea pamoja na mbinu za kufanya doria katika maeneo yenye hatari kubwa ya kutokea kwa moto. A

Aidha, alieleza kuwa elimu hiyo itawasaidia vijana kuwa mabalozi wa usalama wa mazingira katika vijiji vyao.

Baadhi ya vijana walioshiriki mafunzo hayo wameeleza kufurahishwa na fursa waliyoipata wakisema kuwa imewaongezea ujuzi na kuwapa nafasi ya kushiriki moja kwa moja katika shughuli za kulinda misitu.

Walisema maarifa waliyojifunza yatawasaidia kutoa elimu kwa wananchi wengine kuhusu madhara ya moto wa misitu na umuhimu wa kuhifadhi mazingira.

Hatua ya kuwajengea uwezo vijana katika maeneo yanayozunguka Shamba la Miti la Taifa la Sao Hill inaonekana kuwa sehemu muhimu ya mkakati wa kupunguza matukio ya moto wa misitu ambayo yamekuwa yakisababisha hasara kubwa kwa mazingira, uchumi na maendeleo ya jamii.

Serikali na wadau wa uhifadhi wanaamini kuwa ushiriki wa wananchi, hususan vijana, ni nguzo muhimu katika kuhakikisha misitu inalindwa na kuendelea kuwa rasilimali yenye manufaa kwa taifa.









Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) umeendelea kuwa chachu ya mabadiliko kwa kaya maskini, hususan wanawake, kwa kuwawezesha kujikwamua kiuchumi na kuanza maisha ya kujitegemea.

Akizungumza katika kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma jijini Dodoma, Kaimu Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Ndani wa TASAF, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF, Bw. Uswege Edward, amesema taasisi hiyo imewashirikisha baadhi ya wanufaika wa mpango katika banda la maonesho ili kuonesha mafanikio yaliyopatikana kupitia utekelezaji wa TASAF Awamu ya Pili.

Amesema wanufaika hao kutoka Tanzania Bara na Visiwani wameweza kunufaika kwa njia mbalimbali, ikiwemo kupata mitaji, vifaa vya uzalishaji na fursa zilizowasaidia kuanzisha au kuendeleza shughuli za kiuchumi zinazowaingizia kipato.

"Tunajivunia mafanikio ya walengwa wetu maana wakati wa usajili baadhi yao walikuwa wakikabiliwa na changamoto kubwa za maisha, ikiwemo kushindwa kumudu milo mitatu kwa siku. Leo hii wengi wao wanaendesha biashara na shughuli mbalimbali za kiuchumi zinazowapa kipato na kuwafanya wajitegemee", amesema Uswege.

Aidha, amesema TASAF inaamini imefanikiwa kuwasaidia walengwa wengi kuondokana na utegemezi na kuanza safari ya kujitegemea kiuchumi.

Kwa upande wake, mmoja wa wanufaika wa mpango huo, Devota Karia, ameishukuru TASAF kwa kuwapatia nafasi ya kushiriki katika maadhimisho hayo, akieleza kuwa yamekuwa fursa muhimu ya kutangaza biashara zao na kupata wateja wapya.

Pia amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuunga mkono na kuimarisha utekelezaji wa mpango wa TASAF, ambao umeleta matumaini mapya kwa maelfu ya kaya nchini.




 

Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma

Serikali imeeleza mpango wake wa kuimarisha sekta ya korosho nchini kwa kuongeza uwekezaji katika ubanguaji na uchakataji wa zao hilo, lengo likiwa ni kuhakikisha Tanzania inanufaika zaidi kupitia ongezeko la thamani ya mazao yake.

Akijibu swali bungeni Leo, Naibu Waziri wa Kilimo David Silinde lililoulizwa na Abdallah Dadi Chikota kuhusu vivutio kwa wabanguaji wa korosho wa ndani, Serikali imesema inaendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji ili kuvutia zaidi viwanda vya kuchakata korosho ndani ya nchi.

Silinde amesema hatua mbalimbali zimechukuliwa, ikiwemo ujenzi wa Kongani ya Viwanda ya Maranje ambayo imewekewa miundombinu muhimu kama barabara, umeme na maji ili kurahisisha shughuli za uzalishaji na uwekezaji.

Aidha, kongani hiyo imesajiliwa kupitia TISEZA, hatua inayowapa wawekezaji fursa ya kupata vivutio mbalimbali vya kiuwekezaji vinavyotolewa na Serikali.

Serikali imesisitiza kuwa itaendelea kuimarisha mazingira ya sekta ya korosho ili kuongeza kiwango cha ubanguaji ndani ya nchi. Lengo kuu ni kuhakikisha ifikapo mwaka 2030, sehemu kubwa ya korosho zinazozalishwa nchini zinachakatwa hapa nchini, sambamba na kufikia uzalishaji wa hadi tani 1,000,000 kwa mwaka.

Hatua hiyo inalenga kuongeza thamani ya mazao ya ndani, kuimarisha ajira na kuongeza ushindani wa Tanzania katika soko la dunia linalozidi kuhitaji bidhaa zilizopewa thamani zaidi badala ya malighafi.


Na Mwandishi Wetu.

WAKALA wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) umezidi kujipambanua kama muhimili na nguzo madhubuti katika kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa, kupitia mikakati yake endelevu inayolenga kurasimisha shughuli za kiuchumi na kuhakikisha hakuna Mtanzania anayeachwa nyuma katika upatikanaji wa huduma za sajili na leseni.

Hayo yamebainishwa na Ofisa Mtendaji Mkuu wa BRELA, Godfrey Nyaisa, alipokuwa akifungua kikao kazi cha wafanyakazi wa Wakala hiyo kilichofanyika mkoani Morogoro ambapo ametumia nafasi hiyo kuelezea kwa kina mafanikio ya wakala huo katika kuendelea kuwahudumia Watanzania.

“Katika mwaka wa fedha wa 2025/2026, BRELA imefanikiwa kuvuka malengo na kutekeleza majukumu yake ya msingi kwa ufanisi mkubwa ikijikita katika kuboresha huduma kwa wadau, kuimarisha mifumo ya kidijitali, kupanua wigo wa urasimishaji biashara nchini licha ya changamoto za kimazingira na kiuchumi zilizojitokeza” amesema Nyaisa

Kwa upande wake Kaimu Meneja wa Sehemu ya Mipango, Utafiti na Ubunifu wa BRELA Alinda Lema, amebainisha mafanikio hayo yamepatikana kupitia usimamizi thabiti wa Mpango Mkakati wa miaka mitano wa 2021/22–2025/26.

Amefafanua katika kipindi cha kuanzia Julai 2025 hadi Juni 2026, mpango huo umewezesha mazingira ya biashara nchini kwa kuimarisha huduma za sajili na leseni, mifumo ya kiteknolojia, na usimamizi wa utendaji kazi wa watumishi.

Pia kumekuwa na ongezeko la kasi ya urasimishaji wa biashara, kuimarika kwa ulinzi wa haki miliki, na kurahisishwa kwa huduma zote zinazowafikia wadau wa sekta binafsi na ya umma.

“Kampuni zilizosajiliwa nchini zilipanda kutoka 18,541 katika mwaka wa fedha uliopita wa 2024/25 na kufikia kampuni 19,264 katika mwaka wa fedha wa 2025/26, ikiwa ni ongezeko la asilimia 4 linaloakisi kuongezeka kwa imani ya wawekezaji wa ndani na nje.

“Katika urasimishaji wa biashara, usajili wa majina ya biashara uliongezeka kutoka majina 31,123 hadi kufikia 35,362, ikiwa ni ongezeko la asilimia 14,”amesema Lema.

Kwa upande wa sekta ya viwanda na miliki ubunifu nayo haikuachwa nyuma, kwani ilionyesha ukuaji unaochochea azma ya Tanzania kuwa nchi ya viwanda na uchumi wa kati.

Lema ameeleza kuwa utoaji wa leseni za viwanda uliongezeka kwa asilimia 50, kutoka leseni 435 hadi leseni 651 katika kipindi cha mwaka mmoja tu.

Pia utoaji wa Hataza kwa ajili ya kulinda wavumbuzi wa ndani ulishuhudia mapinduzi kwa kuongezeka kutoka hataza 30 hadi 61, ambalo ni ongezeko la asilimia 103, wakati usajili wa alama za biashara na huduma (Trade and Service marks) ukiongezeka kwa asilimia 10 kutoka sajili 3,148 hadi kufikia 3,455, hatua inayolinda alama na ubunifu wa wafanyabiashara sokoni.

BRELA ilitekeleza zoezi la kaguzi elimishi kwa upande wa leseni katika soko kuu la kimkakati la Kariakoo jijini Dar es Salaam. Ukaguzi huo haukulenga kuadhibu, bali kuweka mazingira rafiki ya uendeshaji biashara na uwekezaji kwa kutoa elimu ya uzingatiaji wa sheria za nchi.

Kuhusu uwazi na udhibiti wa mifumo ya kifedha, Wakala huo ulifanikiwa kufanya ukaguzi wa kina wa taarifa za wamiliki manufaa katika mkoa wa Arusha, hatua iliyosaidia kuongeza uelewa na kupunguza makosa yaliyokuwa yanajitokeza katika mfumo wa usajili wa kampuni.

Mkakati huu wa ukaguzi ulienda sambamba na utoaji endelevu wa elimu kwa umma kuanzia Julai 2025 hadi Juni 2026, ambapo BRELA ilitumia mbinu mbalimbali za kisasa kuwafikia wananchi.


Benki ya NMB imetangaza udhamini wa Sh milioni 150 kufanikisha msimu wa nane wa Mashindano ya Kombe la Mkuu wa Majeshi—CDF Cup 2026—yatakayofanyika Dar es Salaam kuanzia Julai 6 hadi 17.

Mashindano hayo yatahusisha michezo 13 na timu kutoka Kamandi ya Makao Makuu ya JWTZ, Kamandi ya Jeshi la Nchi Kavu, Kamandi ya Jeshi la Anga, Kamandi ya Jeshi la Wanamaji, Kamandi ya Jeshi la Akiba na Kamandi ya Jeshi la Kujenga Taifa.

Mkuu wa Idara ya Wateja Binafsi wa Benki ya NMB, Aikansia Muro, alisema udhamini huo unaendeleza ushirikiano wa benki hiyo na majeshi katika kukuza michezo, kuimarisha ushindani na kujenga umoja, afya thabiti na mshikamano miongoni mwa washiriki.

Mashindano yatafunguliwa Julai 6 katika Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, huku yakitarajiwa kutoa jukwaa la kukuza vipaji, kuimarisha utimamu wa mwili na afya ya akili pamoja na kujenga mahusiano mema kwa washiriki.


Mkuu wa Idara ya Wateja Binafsi wa Benki ya NMB, Aikansia Muro (kushoto), akikabidhi hundi mfano ya udhamini wa Sh milioni 150 kwa Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya CDF Cup 2026, Brigedia Jenerali Saidi Hamis Saidi (katikati), jijini Dar es Salaam. Mashindano hayo yatafanyika kuanzia Julai 6 hadi 17, yakishirikisha timu za kijeshi katika michezo 13.


























Dodoma

Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila, amepongeza matumizi ya mfumo wa kisasa wa Supervisory Control and Data Acquisition (SCADA) unaotumiwa na Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA), akisema umeongeza uwazi na ufanisi katika usimamizi wa mafuta nchini.

Dkt. Nguvila alitoa pongezi hizo Juni 23, 2026, alipotembelea banda la PBPA katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali jijini Dodoma na kupata maelezo kuhusu namna mfumo huo unavyofanya kazi.

Alisema matumizi ya teknolojia za kisasa katika sekta ya mafuta yanaisaidia Serikali kufuatilia kwa karibu mwenendo wa mafuta yanayoingia nchini na kuhifadhiwa katika maghala mbalimbali, hivyo kudhibiti upotevu na kuongeza uwajibikaji.

“Ni jambo la kutia moyo kuona taasisi za umma zinatumia teknolojia za kisasa katika kuboresha usimamizi wa rasilimali za taifa. Mfumo huu unasaidia kuongeza uwazi na kuhakikisha mafuta yanayopokelewa yanafika katika maeneo yaliyokusudiwa,” alisema Dkt. Nguvila.

Akitoa maelezo kwa mgeni huyo, Mkaguzi wa Mafuta wa PBPA, Bw. Issa Khamis Mwitazy, alisema mfumo wa SCADA umechangia kwa kiasi kikubwa kudhibiti upotevu wa mafuta ambao kwa muda mrefu ulikuwa changamoto katika sekta hiyo.

Bw. Mwitazy alisema mfumo huo hulinganisha kiwango cha mafuta kilichopokelewa kutoka melini na kiwango kilichofika kwenye maghala, ambapo taarifa hutolewa mara moja endapo kutabainika tofauti yoyote ili hatua za haraka zichukuliwe.

Aidha, alisema mfumo huo unasoma na kufuatilia kwa wakati halisi ujazo wa mafuta kupitia mita za Serikali zilizopo katika bandari za Dar es Salaam, Tanga na Mtwara, pamoja na kusoma kiwango cha mafuta kilichopo katika maghala ya kampuni za mafuta.

Kwa mujibu wa PBPA, matumizi ya mfumo wa SCADA ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuimarisha usimamizi wa mafuta nchini na kuhakikisha sekta hiyo inaendeshwa kwa uwazi, ufanisi na tija zaidi.


NA: DK. REUBENI LUMBAGALA

Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ni chombo muhimu nchini katika kuhakikisha mipango na mikakati ya maendeleo inatimizwa kikamilifu. Hii inatokana na ukweli kuwa mipango mingi ya maendeleo kama uboreshaji wa sekta za elimu, afya, maji, masoko, viwanda, umeme, barabara, makazi, biashara, inategemea upatikanaji wa raslimalifedha ili ziwezeshe utekelezaji wake.

TRA ina wajibu wa kukusanya kodi kutoka kwa walipakodi wake kama wafanyabiashara, wawekezaji, wafanyakazi na wajasiriamali mbalimbali. Mafanikio ya ukusanyaji kodi, ndiyo msingi wa kuiwezesha serikali kutimiza mipango yake ya maendeleo kwa ustawi na maendeleo ya wananchi.

Sasa TRA imetimiza miaka 30 tangu kuanzishwa kwake. TRA imepata mafanikio makubwa sana hasa katika uongozi wa serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.

Rais Dk. Samia aliweka msingi wa serikali yake mapema kwa kuiagiza TRA iwajibike ipasavyo katika kukusanya mapato, lakini mapato hayo yasiwe ya dhuluma. Rais Dk. Samia anataka kila mwananchi mwenye sifa za kulipa kodi alipe.

Aprili 6, 2021, Rais Dk. Samia alipokuwa akiwaapisha makatibu wakuu na manaibu wao, alitoa maelekezo mahsusi kwa TRA. "Kukusanya kodi kwa mabavu havisaidii kwa muda mrefu. Nimepewa takwimu ya zile taskforce (vikosikazi vya kukusanya kodi) mlizoziunda lakini havisaidii, mnawatisha watu wanalazimika kufunga biashara."

"Tunazitaka kodi lakini kodi za dhuluma hapana. Kwa sababu hazitatufikisha mbali. Jinsi ya kurudisha wafanyabiashara, kutengeneza wigo wa kukusanya kodi, nafahamu uamuzi huu niliochukua tutayumba kwa miezi miwili, mitatu lakini baada ya muda tutarudi vizuri," amesema Rais Dk. Samia.

Msisitizo wa kuongeza mapato ulitokana na ukweli kuwa mipango mingi na mizuri aliyonayo Rais Dk. Samia kwa wananchi wake, haitaweza kufanikiwa kama TRA haitakusanya kodi kikamilifu ambayo ndiyo kichochea cha kufanikisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Awali, TRA ilikuwa na utaratibu wa kufunga biashara na shughuli mbalimbali pale ambapo mlipakodi atashindwa kulipa kodi kwa wakati.

Vilevile, katika makadirio ya kodi, baadhi ya wafanyabiashara walikuwa wakilalamikia kuwekewa makadirio makubwa tofauti na kiwango cha biashara zao. Hii iliweka uadui mkubwa kati ya TRA na walipakodi nchini.

MAGEUZI MAKUBWA YAMEONDOA UADUI KATI YA TRA NA WALIPAKODI

Kutokana na maelekezo ya Rais. Dk. Samia kwa TRA, uadui uliokuwepo awali kati ya TRA na walipakodi umeondoka. Hii inatokana na mtazamo chanya alioujenga Rais Dk. Samia kwa pande zote mbili.

Kimsingi, pande zote mbili zinategemeana. TRA anamtegemea mlipakodi kwani pindi kodi inapolipwa ndipo inawezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo ambayo inamnufaisha mlipakodi moja kwa moj.

Rais Dk. Samia akasisitiza pawepo na meza ya mazungumzo na makubaliano ya namna gani mlipakodi atalipa kodi pale ambapo atashindwa kulipa kwa wakati.

Aidha, Rais Samia akasisitiza kuwa kufunga biashara ni kummaliza kabisa mlipakodi kwani biashara yake itakapofungwa, ndipo atashindwa kabisa kulipa kodi kwani hatakuwa na shughuli ya kumuingizia kipato cha kuwezesha kulipa kodi na wala TRA haitaweza kupata kodi yake.

Kongole kwa Kamishna Mkuu wa TRA, Yusuph Mwenda, pamoja na wasaidizi wake nchi nzima wamefanyia kazi maelekezo ya Rais, na sasa tunashuhudia mafanikio ya kumalizika kwa uadui uliokuwepo awali.

Ni faraja kuona tunapoadhimisha miaka 30 ya TRA, kumejengeka uhusiano mzuri kati ya mlipakodi na mamlaka. Hakuna mabavu wala ubabe. Uhusiano mzuri uliopo umewezesha kuongezeka kwa mapato ya serikali.

Mathalani, mwezi Machi, 2026, TRA wamefanikiwa kukusanya trilioni 3.58, na kimsingi, ongezeko la makusanyo yamewezesha hata bajeti ya mwaka 2026/2027, kutegemea mapato ya ndani kwa asilimia 74.2.


Maoni : 0620 800 462


Na Janeth Raphael MichuziTv 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Prof. Riziki Shemdoe, ametoa maagizo ya kuchukuliwa hatua kwa maafisa rasilimali watu watakaobainika kusababisha ucheleweshaji wa upandishaji madaraja kwa watumishi wa umma, licha ya wahusika hao kutimiza vigezo vyote vinavyohitajika.

Prof. Shemdoe ametoa kauli hiyo leo wakati akifunga Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma jijini Dodoma, kwa niaba ya Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dkt. Moses Kusiluka.

Amesema kumekuwepo na changamoto ya baadhi ya maafisa rasilimali watu kushindwa kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi, hali inayosababisha watumishi stahiki kukosa au kucheleweshwa kupanda madaraja kupitia mifumo ya kiutumishi.

“Watumishi wanaostahili kupandishwa vyeo hawapaswi kukosa haki zao kutokana na uzembe wa kiutendaji wa mtu mmoja,” amesisitiza.

Katika hatua nyingine, Prof. Shemdoe ameeleza kuwa hata yeye binafsi aliwahi kukumbana na changamoto ya kucheleweshwa kupandishwa cheo kwa takribani mwaka mmoja kutokana na kutokukamilika kwa taratibu za kiutumishi kwa wakati.

Aidha, ameelekeza kufanyika kwa tathmini maalum kwa maafisa rasilimali watu wakuu wote waliohusika na ucheleweshaji wa upandishaji madaraja katika mwaka wa fedha 2025/2026, ili hatua stahiki zichukuliwe dhidi ya waliobainika na uzembe.

Prof. Shemdoe pia amewataka waajiri kuhakikisha wanatenga bajeti ya kushiriki Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, huku akisisitiza umuhimu wa maonesho hayo katika kuboresha utoaji huduma kwa wananchi.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora (OR-MUUUB), Bw. Juma Mkomi, amesema maadhimisho hayo ni sehemu ya utekelezaji wa azimio la Umoja wa Afrika linalolenga kuenzi Siku ya Utumishi wa Umma Barani Afrika.

Ameongeza kuwa lengo la maadhimisho hayo ni kutambua mchango wa watumishi wa umma katika maendeleo ya taifa, kuhamasisha ubunifu katika utoaji huduma, pamoja na kukusanya maoni ya wananchi kuhusu ubora wa huduma zinazotolewa na taasisi za umma.










Top News