Na Byera Deus, Bukoba

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Bukoba, Fatna Laay, amesema Halmashauri hiyo imeongeza upeo wa kukusanya mapato ya ndani ambapo kuanzia Julai hadi Machi katika mwaka wa fedha 2025/2026 wamekusanya shilingi bilioni 4.2 sawa na asilimia 94.

Amesema ongezeko hilo ni sawa na asilimia 19 ya robo ya tatu ya mwaka wa fedha, na matarajio ni ukusanyaji wa mapato ya ndani kukamilika kwa asilimia 100 kabla ya mwaka mpya wa fedha kuanza, yaani 2026/2027.

Ameeleza kuwa mpaka sasa zaidi ya bilioni moja zilizokusanywa kutoka kwenye mapato ya ndani zimerudi kwa wananchi kukuza uchumi wao na kuchangia miradi mbalimbali ya maendeleo.

Aidha Halmashauri hiyo inaendelea kuboresha kikosi cha kukusanya mapato ya ndani kwa kuimarisha vifaa na mifumo ya ukusanyaji pamoja na kubadili mbinu mpya kila siku ili kuondoa mazoea pamoja na kutekeleza kwa kina sheria za Halmashauri za ukusanyaji mapato.

Pia  miradi ya kimkakati iliyopitishwa na Baraza la Madiwani, ambayo inaenda kuimarisha uchumi wa wananchi na kuongeza ajira kwa vijana, inaendelea kutekelezwa kwa kishindo.

Miradi hiyo ni ujenzi wa soko la ndizi Kemondo wenye thamani ya shilingi milioni 150, mradi wa kitega uchumi Shablidini wenye thamani ya shilingi bilioni 1.2, na mradi wa ujenzi wa ghala na mtambo wa kukausha dagaa wenye thamani ya shilingi milioni 382.

Akizungumza Mkuu wa Wilaya ya Bukoba, Erasto Sima, ametoa wito kwa timu ya ukusanyaji kutoacha nafasi yoyote kwa sehemu zinazoweza kuongeza mapato ya ndani huku akidai kuwa kwa sasa matunda ya ukusanyaji wa mapato ya ndani yameanza kustawisha jamii baada ya fedha kuanza kupelekwa kwenye miradi ya maendeleo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Sadothi Ijunga, alipongeza namna mkurugenzi wa Halmashauri hiyo anavyosimamia utekelezaji wa miradi ya serikali na kusema kuwa atawasimamia madiwani na kuendelea kuwashirikisha namna ya kusimama pamoja kwa ajili ya kuibua vyanzo vya mapato ya ndani na ushiriki wa miradi ya maendeleo katika maeneo yao.







Na.Ashura Mohamed - Arusha

Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) kwa kushirikiana na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), wametoa vitanda 160 pamoja na magodoro 160 vyenye thamani ya shilingi milioni 43,kwa ajili ya kusaidia waraibu wa dawa za kulevya wanaopata huduma katika nyumba za upatikanaji nafuu (Sober House),zinazoratibiwa na Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) Kanda ya Kaskazini.

Akizungumza katika hafla hiyo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF, Dkt.Fortunatus Magambo bw. Venance Mwaijibe,amesema msaada huo ni utaratibu wa taasisi hiyo wa kusaidia jamii ambapo awamu hii imewaangukia waraibu wa Madawa ya Kulevya Jijini Arusha.

Bw.Venance amesema kuwa kazi kubwa ya mfuko wa jamii ni kukaa na jamii kwa kuwa PSSSF ni mfuko wa jamii na Waraibu wa Madawa ya kulevya ni wanajamii wenzao hivyo wana wajibu wa kuwashika mikono ili kwenda sambamba na kauli mbiu ya serikali ya Kazi na Utu ili kufanya kazi kwa kujali utu,na kuhakikisha waraibu wanapambana na changamoto hiyo.

"Niseme tu PSSSF itaendelea kuwa karibu na Jamii na tutaendelea kuiunga mkono serikali yetu kwa kuendelea kuisadia jamii katatua baadhi ya changamoto sehemu nyingine tumejenga madasa,pia tumechimba visima na leo hii ni vitanda 160 na magodoro 160,ili kuwawezesha hawa wenzetu kuwa na mazingira bora ili wapone kabisa"Alisisitiza Venance

Amesema PSSSF imeamua kuunga mkono juhudi za serikali kwa kutoa vitanda na magodoro hayo ili kuboresha huduma za malazi kwa waraibu wanaopatiwa matibabu na ushauri nasaha kwani mfuko huo unaamini katika kushirikiana na jamii kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi.

“PSSSF tuna kauli mbiu ya ‘Leo, Kesho’. Kwa kushirikiana na NSSF tunajenga maisha ya sasa na ya baadaye, tumeungana kurejesha kwa jamii sehemu ya faida tunazopata kwa kusaidia mapambano dhidi ya dawa za kulevya ili kupata raia wema na wenye mchango chanya kwa taifa,” Alifafanua Venance

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Abubakar Mshangama, kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa mfuko huo, Masha Mshomba, alisema mifuko hiyo miwili imeamua kushirikiana kuunga mkono juhudi za serikali katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya.

Bi.Sarah Ndaba, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa DCEA, Aretus Lyimo ameishukuru PSSSF na NSSF kwa msaada huo,akisema utasaidia kuimarisha huduma zinazotolewa kwa waraibu wanaopata nafuu kupitia nyumba hizo.

“Msaada huu utasaidia waraibu kurejea katika hali zao za kawaida na taasisi hizi zimetusaidia sana kuboresha mazingira ya waraibu wetu katika makazi yao hivyo tunaomba na wadau wengine wajitokeze kusaidia juhudi hizi kwa kuwa mazingira bora ya matibabu yanaongeza uwezekano wa mgonjwa kupona na kurejea katika maisha ya kawaida,” Alisema Sarah

Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha, ambaye ndie alikuwa awe Mgeni rasmi katika hafla hiyo CPA Amos Makalla, Mkuu wa Wilaya ya Arusha, Joseph Mkude, amesema mapambano dhidi ya dawa za kulevya yanawezekana kupitia ushirikiano wa wadau mbalimbali.

Amesema DCEA inaendelea kudhibiti biashara ya dawa za kulevya pamoja na kuhakikisha huduma za matibabu zinapatikana katika vituo mbalimbali hivyo kama serikali ni lazima kulinda nguvu kazi ya taifa.

Baadhi ya waraibu waliopona Baita Chacha amesema alitumia dawa za kulevya kwa miaka 15 kabla ya kupata msaada kupitia Sober House, ambapo sasa amepona baada ya kuishi katika kituo hicho kwa mwaka mmoja kwani uraibu ni changamoto ya afya ya akili inayohitaji msaada wa karibu kutoka kwa jamii na wataalamu.

Mkoa wa Arusha una jumla ya nyumba 19 zinazotoa huduma kwa waraibu ambapo katika mkoa huo kuna waraibu wapatao 505,wanawake ni 98 na wanaume ni 407.















 

Wananchi wa Jiji la Dar es Salaam wanatarajiwa kushuhudia uzinduzi wa kampeni maalum ya kitaifa ijulikanayo kama Muungano Caravan, yenye lengo la kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa Muungano wa Tanzania pamoja na kuhamasisha uzalendo, mshikamano wa kitaifa na ushiriki wa wananchi katika maendeleo ya nchi.

Uzinduzi huo unatarajiwa kufanyika katika maeneo mbalimbali ya Dar es Salaam, huku mamia ya wananchi, vijana, viongozi wa serikali, wadau wa maendeleo, wanafunzi pamoja na makundi mbalimbali ya kijamii wakitarajiwa kushiriki kwa wingi katika shughuli hiyo muhimu ya kitaifa.

Kwa mujibu wa waandaaji wa kampeni hiyo, Muungano Caravan ni jukwaa maalum litakalowakutanisha wananchi kutoka makundi tofauti ili kupata elimu kuhusu historia ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, mafanikio yaliyopatikana tangu kuanzishwa kwake, pamoja na nafasi ya wananchi katika kuuenzi na kuulinda Muungano huo kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Wadau hao wameeleza kuwa vijana ndio walengwa wakuu wa kampeni hiyo kutokana na umuhimu wa kuwajengea uelewa mpana kuhusu tunu za taifa, historia ya nchi na wajibu wao katika kudumisha amani na umoja wa Watanzania.

Kupitia maonesho mbalimbali, mijadala ya wazi, semina za elimu ya uraia na vipindi vya maswali na majibu, wananchi watapata nafasi ya kujifunza kwa kina kuhusu hatua zilizopigwa katika sekta mbalimbali kutokana na Muungano ikiwemo elimu, biashara, uwekezaji, michezo, utamaduni na maendeleo ya kijamii.

Aidha, waandaaji wamebainisha kuwa vijana wengi wamekuwa wakihitaji elimu ya kina kuhusu Muungano ili waweze kuelewa chimbuko lake, faida zake na changamoto zinazoweza kujitokeza. Kupitia kampeni hiyo, vijana watapata nafasi ya kuuliza maswali moja kwa moja kwa wataalamu na viongozi wanaohusika na masuala ya Muungano.

Mbali na elimu hiyo, washiriki watapata nafasi ya kushiriki katika Muungano Challenge, shindano maalum litakalotoa zawadi mbalimbali kwa washiriki watakaofanya vizuri katika maswali yanayohusu Muungano, uzalendo, historia ya Tanzania na masuala ya maendeleo ya taifa.

Tamasha hilo pia linatarajiwa kupambwa na burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali maarufu nchini, vikundi vya ngoma za asili, muziki wa kizazi kipya pamoja na sanaa za maonesho zitakazobeba ujumbe wa umoja, amani na uzalendo.

Katika kuhakikisha ujumbe unawafikia wananchi wengi zaidi, msafara wa Muungano Caravan utaendelea katika wilaya mbalimbali za Dar es Salaam zikiwemo Ilala, Temeke, Kinondoni, Kigamboni na Ubungo. Kila eneo litakuwa na programu maalum za elimu, burudani na ushiriki wa wananchi ili kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa Muungano katika maendeleo ya taifa.

Akizungumza kuhusu kampeni hiyo, mmoja wa waratibu alisema kuwa dhamira kuu ni kujenga kizazi chenye uelewa wa historia ya taifa lao na kinachothamini amani, umoja na mshikamano uliopo nchini.

“Tunataka vijana wawe mstari wa mbele katika kuujua na kuuenzi Muungano wetu. Elimu hii ni muhimu kwa sababu vijana ndio viongozi wa kesho, hivyo wanapaswa kuelewa mchango wa Muungano katika kulinda amani na kuleta maendeleo ya taifa letu,” alisema.

Aidha, viongozi mbalimbali wa kijamii na wadau wa maendeleo wamepongeza kuanzishwa kwa kampeni hiyo wakisema kuwa itasaidia kuimarisha mshikamano wa kitaifa na kuongeza uelewa kwa wananchi kuhusu masuala ya Muungano ambayo kwa muda mrefu yamekuwa yakihitaji elimu zaidi hasa kwa kizazi cha vijana.

Kaulimbiu ya kampeni hiyo ni:
“Safari ya Umoja – Tudumishe Muungano Wetu kwa Maendeleo Endelevu.”

Wananchi wametakiwa kujitokeza kwa wingi kushiriki katika uzinduzi huo ambao unatarajiwa kuwa mwanzo wa harakati mpya za kuendeleza uzalendo, elimu ya uraia na mshikamano wa kitaifa nchini Tanzania.




 





Waziri wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (Mb), leo tarehe 6 Mei, 2026 amefungua rasmi Mkutano Mkuu wa Pili wa Mwaka wa Jumuiya ya Wataalamu wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu katika Utumishi wa Umma (AAPAM), unaowakutanisha wadau mbalimbali wa sekta hiyo.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano huo uliofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC), Waziri Ridhiwani alisisitiza umuhimu wa wataalamu wa Rasilimali watu katika kuimarisha utendaji na ufanisi wa taasisi za umma ambapo alibainisha kuwa mchango wao ni muhimu katika kufanikisha utoaji wa huduma bora ili kuendana na kasi ya mabadiliko ya kiutawala na kiteknolojia.

Aidha, alieleza kuwa Serikali inaendelea kuweka mazingira rafiki kwa wataalamu hao ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa weledi.


Katika ziara yake katika mabanda ya maonesho yanayoambatana na mkutano huo, Mhe. Ridhiwani alitembelea banda la Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), ambapo alipata fursa ya kujionea shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na taasisi hiyo pamoja na maboresho ya huduma zake.


Meneja Masoko na Uhusiano kwa Umma TEMESA Bi Martha Joachim akimkabidhi zawadi Waziri wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (Mb)



Akiwa katika banda hilo, aliipongeza TEMESA kwa kumpata Mtendaji Mkuu mpya, nakusema hatua hiyo imeashiria fursa ya kuimarisha zaidi uongozi, kuongeza ubunifu na kuleta matokeo chanya katika utoaji wa huduma kwa umma.


“TEMESA kwanza nawapongeza kwa kupata mtendaji mpya naamini mabadiliko haya yataleta chachu ya kiutendaji na utoaji wa huduma bora hongereni sana.” Amesema Mhe. Ridhiwani.


Mkutano huo wa siku nne umebeba kaulimbiu isemayo: “Kufikiri upya utoaji wa huduma kwa umma: Jinsi Serikali inavyoweza kutumia teknolojia kuanzisha huduma bora na zinazomlenga mwananchi, kukabiliana na ukosefu wa ajira kwa vijana pamoja na changamoto za mazingira.”

Meneja wa Kanda Namba Sita, Halmashauri ya Jiji la Dodoma Lucas Nkelege amekutana na watendaji wa kata pamoja na watendaji wa mitaa inayounda kanda hiyo kwa lengo la kutoa elimu ya vyanzo vya mapato na kuwakumbusha umuhimu wa ukusanyaji wa mapato kwa wakati ili kuongeza ufanisi wa huduma kwa wananchi.

Akizungumza katika kikao hicho, Nkelege ameeleza kuwa mapato yanayokusanywa katika maeneo mbalimbali ndiyo msingi wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo pamoja na kuboresha huduma muhimu za jamii ikiwemo usafi wa mazingira, ujenzi wa miundombinu na huduma za kijamii.

Amesisitiza kuwa watendaji wanapaswa kuwa mstari wa mbele katika kutoa elimu kwa wananchi kuhusu ulipaji wa tozo na ada mbalimbali kwa hiari na kwa kuzingatia taratibu zilizowekwa, huku akiongeza kuwa ukusanyaji wa mapato ni jukumu la pamoja linalohitaji ushirikiano wa karibu kati ya watendaji wa kata, mitaa na viongozi wa serikali za mitaa. 

“Ukusanyaji wa mapato si kazi ya mtu mmoja, ni jukumu la pamoja. Tukishirikiana kwa karibu, tutakusanya mapato kwa ufanisi na kuleta maendeleo ya haraka kwa wananchi wetu” alisema Nkelege.

Watendaji wanahimizwa kutambua na kusimamia vyanzo vyote vya mapato vilivyopo kwenye maeneo yao ikiwemo biashara ndogondogo, ushuru wa huduma, ada za vibali na vyanzo vingine halali vya mapato ili kuzuia upotevu wa mapato.







Nimezungumza na maafisa tawala na RasilimaliWatu , katika mkutano uliofanyika Ukumbi wa AICC, Arusha na kuwakumbusha kutekeleza wajibu wao na kuleta furaha kwa watumishi wa umma ili kwa upande mwengine nao wapeleke furaha na neema kwa Watanzania . Nimeyaeleza hayo kufuatia maamuzi mbalimbali yanayofanywa na serikali ya awamu ya sita katika kuhakikisha maslahi ya Watumishi wa umma nchini yanaboreka.

Uamuzi wa hivi karibuni wa Serikali kupandisha madaraja watumishi 219,042 ni hatua ya kihistoria katika kuimarisha utumishi wa umma nchini Tanzania. Hatua hii ambayo imepata ridhaa ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na ongezeko la mishahara ya watumishi wa umma (2025): +35.1% , Ongezeko la kima cha chini sekta binafsi (2025/26): +33.4% , ambapo Sekta mbalimbali zinakwenda athiriwa na maboresho haya ikiwemo afya, elimu, kilimo, mawasiliano, usafirishaji, nishati, viwanda, biashara, hoteli, michezo, uvuvi, baharini, madini ,utamaduni n.k

Matokeo haya kitakwimu zinaonyesha kasi ya mageuzi ya kiutumishi chini ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan ambayo inaonyesha uongozi wa kimkakati unaoweka mbele ustawi wa watumishi na ufanisi wa taasisi za umma.





📍 Apandisha mishahara kwa asilimia 35


Na Mwandishi Wetu, Arusha

SERIKALI ya Awamu ya Sita imefanya mageuzi makubwa ya kiutumishi nchini kwa kupandisha madaraja watumishi wa umma 219,042, huku ikiongeza mishahara kwa asilimia 35.1, hatua inayotajwa kuwa ni kielelezo cha uongozi unaoweka mbele ustawi wa mfanyakazi.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete, ameyabainisha hayo leo jijini Arusha wakati akizungumza na Maafisa Tawala na Rasilimali Watu katika mkutano uliofanyika Ukumbi wa AICC.

Mhe. Kikwete alisema maamuzi hayo ya kimkakati yaliyopata ridhaa ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, yanalenga kuleta "furaha na neema" kwa watumishi wa umma ili nao waweze kutoa huduma bora na kupeleka furaha kwa Watanzania wote kupitia utendaji wao.

Ongezeko la Mishahara na Sekta Binafsi

Akifafanua kuhusu neema hiyo ya kiutumishi, Waziri Kikwete alibainisha kuwa mbali na ongezeko la 35.1% kwa watumishi wa umma mwaka 2025, Serikali pia imeimarisha sekta binafsi kwa kuongeza kima cha chini cha mishahara kwa 33.4% kwa mwaka wa fedha 2025/26.

Alisema maboresho hayo yanagusa sekta mbalimbali za kimkakati nchini ikiwemo Afya, Elimu, Kilimo, Mawasiliano, Usafirishaji, Nishati, Viwanda, Biashara, Madini, na Utalii.

"Nimezungumza na maafisa rasilimali watu na kuwakumbusha kutekeleza wajibu wao wa kuleta furaha kwa watumishi. Uamuzi wa Rais Samia kupandisha madaraja watumishi zaidi ya laki mbili ni hatua ya kihistoria katika kuimarisha utumishi wa umma nchini Tanzania," alisema Waziri Kikwete.

Waziri Kikwete aliongeza kuwa takwimu hizo zinaonyesha kasi ya mageuzi chini ya uongozi wa Rais Samia, ambaye amedhihirisha kwa vitendo kuwa ufanisi wa taasisi za umma unategemea sana kuimarika kwa maslahi na hali ya maisha ya watumishi.

Aliwataka Maafisa Tawala nchini kuhakikisha wanatekeleza maelekezo ya Serikali kwa uadilifu ili watumishi wapate haki zao kwa wakati, jambo litakaloongeza morali ya kazi na tija katika kuwahudumia wananchi.





Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na shirika la kimataifa la Brooke East Africa, inatarajia kuhitimisha kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Punda Kitaifa hapo kesho.

Hafla hiyo ya kimkakati imepangwa kufanyika katika Kata ya Mgusu, iliyopo ndani ya Halmashauri ya Manispaa ya Geita, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kitaifa za kutambua mchango wa mnyama huyu katika uchumi.

Uamuzi wa kuifanya Kata ya Mgusu kuwa kitovu cha maadhimisho haya umechangiwa na takwimu za kijiografia na kiuchumi zinazoonyesha mwingiliano mkubwa kati ya jamii na punda.

Afisa Mifugo kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bi. Tabitha Kitingu, amebainisha kuwa eneo hilo lina idadi kubwa ya punda ambao ni kiungo muhimu katika mnyororo wa uzalishaji, hususan kwenye shughuli za uchimbaji madini.

Kwa mujibu wa tathmini za kitaalamu, Kata ya Mgusu pekee inakadiriwa kuwa na idadi inayozidi Punda 500.

Kutokana na idadi hiyo kubwa, Serikali imeona umuhimu wa kutoa kipaumbele katika utoaji wa elimu ya kina kwa wamiliki na watumiaji wa wanyama hao, lengo likiwa ni kuhakikisha punda wanapata huduma bora na stahiki kulingana na miongozo ya ustawi wa wanyama duniani.

Msingi mkuu wa maadhimisho haya ni kusisitiza haki za msingi za mnyama kazi, ambazo mara nyingi hupuuzwa kutokana na shinikizo la shughuli za kiuchumi migodini.

Elimu itakayotolewa inalenga kubadilisha mitazamo ya wafugaji ili wajali afya, lishe, na mapumziko ya punda, jambo ambalo ni muhimu katika kuongeza tija na uendelevu wa nguvu kazi ya mnyama huyo.

Kwa upande wake, Daktari wa Mifugo kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Geita, Dkt. David Misonge, amethibitisha kuwa wataalamu wa afya ya wanyama wamekusanywa kutoka maeneo mbalimbali mkoani humo.

Kikosi hicho cha wataalamu kimejipanga kutoa huduma za kitabibu na ushauri wa kitaalamu, hasa katika maeneo ya migodi ambapo punda hukabiliwa na changamoto nyingi za kiafya kutokana na kubeba mizigo mizito.

Maadhimisho haya pia yanajumuisha zoezi la uchunguzi wa afya na matibabu ya punda wenye magonjwa na majeraha mbalimbali yanayotokana na mazingira yao ya kazi.

Hatua hii ni sehemu ya mkakati mpana wa Serikali mkoani Geita wa kudhibiti maradhi ya mlipuko miongoni mwa mifugo na kuhakikisha kuwa mnyama kazi hapati mateso yasiyo ya lazima wakati wa utekelezaji wa majukumu yake.

Aidha, Serikali imesisitiza dhamira yake ya dhati ya kuendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo katika kutoa elimu endelevu kwa wananchi.

Lengo ni kujenga jamii yenye uelewa wa kisheria na kimaadili kuhusu utunzaji wa wanyama, ili kuondoa kabisa vitendo vya ukatili na kuhakikisha punda wanatibiwa kwa wakati wanapougua.

Kwa upande mwingine, jamii ya wafugaji na wakazi wa Geita wametoa shukrani zao za dhati kwa mashirika ya Brooke East Africa na ASPRA kwa mchango wao thabiti.

Mashirika haya yamekuwa mstari wa mbele katika kutoa matibabu ya ruzuku na mafunzo ya mbinu bora za ufugaji, hali inayochochea mabadiliko chanya ya kijamii na kiuchumi katika mkoa wa Geita.





Serikali itaendelea kuimarisha usimamizi na maendeleo ya taaluma ya ualimu nchini kupitia utekelezaji wa majukumu ya Bodi ya Kitaalamu ya Walimu Tanzania (Tanzania Teachers Professional Board), ikiwa ni sehemu ya juhudi za kulinda na kuinua hadhi ya taaluma hiyo.

Kupitia hatua hiyo, Serikali itaandaa mwongozo wa viwango vya ufundishaji ili kukuza mafunzo endelevu kwa walimu, pamoja na kuandaa Mwongozo wa Maadili na Mwenendo wa Taaluma ya Ualimu utakaosaidia kuimarisha nidhamu na weledi katika sekta ya elimu.

Hayo yameelezwa bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara yake kwa mwaka wa fedha 2026/27.

Katika hatua nyingine, Serikali itaanza kutekeleza mpango wa mafunzo kwa vitendo wa mwaka mmoja (internship) kwa wahitimu wa mafunzo ya ualimu, hatua inayolenga kuwawezesha walimu tarajali kuoanisha maarifa ya nadharia na uhalisia wa kazi darasani.

Aidha, Serikali itaendelea kuwajengea uwezo walimu wa shule za msingi na sekondari, wakufunzi wa vyuo vya ualimu, wathibiti ubora wa shule na wasimamizi wa elimu ili kuboresha utendaji katika sekta ya elimu.

Katika mpango huo, walimu 1,223 watanufaika na ufadhili wa masomo ya Stashahada ya Ualimu wa Elimu Maalum, huku walimu 3,000 wakipatiwa mafunzo ya ushauri na unasihi kuhusu malezi, stadi za maisha na ulinzi wa mtoto.

Vilevile, watendaji 5,500 pamoja na walimu na wanafunzi watanufaika na mafunzo kuhusu matumizi ya majukwaa ya kielimu, ikiwemo maktaba mtandao na majukwaa ya kujifunza mtandaoni kwa lengo la kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika elimu.



WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa Kikao Kazi cha 21 cha Maafisa Habari, Mawasiliano, Itifaki na Uhusiano Serikalini Mei leo 7, 2026 mkoani Njombe.

Kikao kazi hicho cha mwaka, kinawakutanisha zaidi ya Maafisa Habari 300 kutoka taasisi mbalimbali za Serikali kote nchini kwa lengo la kuwanoa na kuwajengea uwezo, kusimamia na kuzifikisha kwa ufanisi taarifa za Serikali kwa umma.

Kupitia kikaokazi hicho washiriki watapata mafunzo na kufanya mijadala mizito ikiwemo ya uandishi wa kisasa wa taarifa kwa umma, mbinu za kuandika makala zenye mvuto magazetini pamoja na kanuni muhimu za itifaki katika shughuli za kitaifa.

Aidha, watapata fursa ya kujifunza kuhusu matumizi sahihi ya picha za viongozi, utaratibu wa utajo rasmi na suala la mwonekano wa mavazi katika mikutano ya kitaifa na kimataifa

Katika hatua ya kuimarisha mawasiliano ya Serikali hadi ngazi za chini, washiriki wameendelea kuhimizwa kushirikiana kwa karibu na redio za kijamii pamoja na klabu za waandishi wa habari mikoani ili kuongeza ufanisi wa utoaji wa taarifa kwa wananchi.

Sambamba na kikao hicho, wananchi wa Mkoa wa Njombe wananufaika na huduma za kibingwa bobezi zinazotolewa na wataalamu kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili (Upanga na Mloganzila) pamoja na Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Ubongo Muhimbili (MOI).

Mbali na mafunzo hayo, washiriki pia watapata fursa ya kutembelea kiwanda cha AVO AFRICA kinachozalisha mafuta ya parachichi, kushuhudia vivutio vya asili ikiwemo maporomoko ya maji ya Mpanga Kipengele, na kushiriki zoezi la upandaji miti kulinda vyanzo vya maji katika Halmashauri ya Mji wa Njombe.

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan aongoza Kikao cha kawaida cha Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kilichoketi mkoani Dodoma tarehe 07 Mei 2026.

Top News