-Wasema unaongeza uwazi, ufanisi na kuokoa muda wa kupata huduma


Na Grace Michael, Dar es Salaam

WANANCHI na wanachama wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) wamepongeza Mfumo wa Kujihudumia Binafsi (Self Service) unaowezesha wanachama kupata huduma mbalimbali kupitia simu janja, wakisema mfumo huo umeongeza uwazi katika utoaji wa huduma, kurahisisha upatikanaji wa taarifa na kuokoa muda ambao awali walilazimika kuutumia kufika katika ofisi za NHIF.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti walipotembelea banda la NHIF katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, wananchi hao walisema maboresho ya mifumo ya kidijitali ya NHIF yameongeza ufanisi na kuimarisha usimamizi wa huduma za bima ya afya.

Bw. Emmanuel Selemani alisema mfumo huo unampa mwanachama uwezo wa kuona historia ya huduma zote alizopata katika vituo vya kutolea huduma za afya, hatua inayochangia kuongeza uwazi na kuwapa wanachama nafasi ya kushiriki katika kulinda rasilimali za Mfuko.

"Mfumo huu ni mzuri sana kwa sababu kila mwanachama anaweza kuona huduma alizopata katika kituo cha afya. Ikitokea kuna huduma zimeonekana kwenye mfumo lakini hakuzipata, anaweza kutoa taarifa NHIF ili zifuatiliwe. Hii itasaidia kudhibiti na kuzuia vitendo vya udanganyifu katika utoaji wa huduma," alisema.

Kwa upande wake, Bi. Maria Nzalima alisema ameridhishwa na huduma zinazotolewa katika banda la NHIF kwenye maonesho hayo kutokana na kasi ya utoaji wa huduma pamoja na elimu aliyopata kuhusu haki na wajibu wa mwanachama wa NHIF.

"Huduma ni za haraka na nimepata elimu muhimu kuhusu namna ya kutumia bima yangu pamoja na haki na wajibu wangu kama mwanachama. Hii imeniongezea uelewa na kujiamini ninapotumia huduma za NHIF," alisema.

Akizungumza kuhusu huduma zinazotolewa katika banda la NHIF, Ofisa Uanachama Mwandamizi, Bw. Hassan Ally, alisema wananchi wanapata huduma mbalimbali ikiwemo usajili kupitia vifurushi mbalimbali vya bima ya afya, elimu ya matumizi ya Mfumo wa Self Service, uhuishaji wa taarifa za wanachama, kubadilisha namba za simu pamoja na kuunganisha taarifa zao na Mfumo wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA).

Aliongeza kuwa maonesho hayo yanatoa fursa muhimu kwa wananchi kupata elimu kuhusu huduma za NHIF na kujisajili ili waweze kunufaika na huduma za bima ya afya.

"Tunawahamasisha wananchi wote kutembelea banda la NHIF lililopo ndani ya Banda la Kijiji cha Bima ili kupata elimu, kujisajili na kufahamu huduma mbalimbali zinazotolewa na Mfuko kwa wanachama wake," alisema.

NHIF imeendelea kushiriki Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam kila mwaka ikiwa ni sehemu ya jitihada za kusogeza huduma kwa wananchi, kutoa elimu kuhusu bima ya afya na kuhamasisha ushiriki katika utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote. ”Bima ya Afya kwa Wote, Jiunge Sasa."






KATIKA kuhakikisha vijana wanawekwa viti vya mbele katika ajenda ya uchumi Serikali  inaandaa maboresho ya kisera na kisheria yatakayowaondolea vijana wajasiriamali kikwazo cha muda mrefu cha ukosefu wa dhamana za mikopo kwa kuimarisha mfumo wa udhamini wa mikopo na kuruhusu matumizi ya dhamana zinazohamishika.

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam alipomwakilisha Rais wa Serikali ya Jamuhuri Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati wa hafla ya kuwatambua na kukabidhi zawadi kwa washindi wa shindano la ‘Vijana Uchumi Challenge’ Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amesema; Serikali inatambua kundi la vijana na kuwepo kwa Wizara maalum inayoshughulikia masuala ya vijana ni moja ya mkakati wa kuhakikisha kuelekea uchumi endelevu vijana wanakuwa sehemu ya mafanikio hayo kupitia mawazo na ubunifu yenye kutatua changamoto za kijamii na uchumi.

Amesema; Serikali inaandaa maboresho ya kisera na kisheria yatakayowaondolea vijana wajasiriamali kikwazo cha muda mrefu cha ukosefu wa dhamana ya mikopo kwa kuimarisha mfumo wa udhamini wa mikopo na kuruhusu matumizi ya dhamana zinazohamishika.

“Tunataka kuhalalisha matumizi ya dhamana zinazohamishika. Kwa mfano, mkulima au mfugaji anayetumia stakabadhi ghalani aweze kuitumia hiyo kupata mkopo wa pembejeo bila kusubiri kuuza mazao yake,” ameeleza.

Amesema Benki Kuu ya Tanzania (BoT) tayari ina dirisha la udhamini wa mikopo kwa biashara ndogo, za kati na kubwa, ambalo linaendelea kuboreshwa na litabadilishwa kuwa taasisi maalum itakayoratibu masuala ya udhamini wa mikopo nchini.

“Tayari kuna zaidi ya shilingi Bilioni 280 kwa ajili ya jukumu hilo, na wadau wengine wameonesha nia ya kushiriki kwa kiwango cha zaidi ya dola za Marekani milioni 150. Hizi zitasaidia biashara ndogo, za kati na biashara kubwa kupata udhamini wa mikopo,” ameeleza Dkt. Nchemba.

Aidha Waziri Mkuu ameeleza kuwa;  hatua hizo zinaenda sambamba na maboresho mengine ya kisheria yaliyofanywa na Serikali, ikiwemo kuondoa sharti lililokuwa likiwazuia watanzania kuwa wakandarasi wakuu wa miradi mikubwa, hatua inayopanua fursa za ushiriki wa wazawa katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo hususani kundi la vijana.

Pia Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - Maendeleo ya Vijana Dkt. Joel Nanauka amesema; Serikali inawatambua vijana, kuwasikiliza pamoja na kuwaweka katika ajenda za maendeleo ya kitaifa ikiwemo kutoa fursa za ajira na ujasiriamali.

“Tumekusanyika ili kutambua na kusherehekea ubunifu, bidii na ujasiri wa vijana wetu katika Vijana Uchumi Challenge – Mpango ambao unalenga kuwawezesha vijana kuwa wajasiriamali na wabunifu katika uchumi wa Taifa, kwa kuwa tunatambua vijana ndio nguvu ya Taifa na ndio wabebaji wa maendeleo ya kesho.” Amesema.

Aidha ameeleza kuwa Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuwaweka vijana viti vya mbele katika agenda ya uchumi na kupitia shindano hilo vijana wamepata fursa ya kutoa maoni yao, kuwasilisha biashara zao na kuonyesha uwezo wao.

“Leo, tunawapa heshima vijana ambao wamethubutu, wamefanya kazi kwa bidii, na wameonyesha kuwa hata katika changamoto za kiuchumi, wanaweza kujenga suluhisho.” Amesema.

Aidha amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kuwaunga mkono kupitia mikopo nafuu, mafunzo, fursa za ajira na ushirikiano na sekta binafsi ili kuliinua kundi hilo muhimu katika ustawi wa Taifa kiuchumi na jamii.

Akifafanua kuhusu shindano hilo Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana Jenifa  Omolo amesema shindano la “Vijana Uchumi Challenge lililobeba kauli mbiu ya ‘Wana Tunafikiri, Taifa Linasonga’ limekuwa jukwaa muhimu na limetoa nafasi ya kuibua fikra na ubunifu wa vijana, kujenga ujasiri, na kuonyesha kuwa vijana wana nafasi kubwa katika kubuni suluhisho za changamoto za kiuchumi na kijamii. 

Amesema kuwa shindano hilo ni sehemu ya dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuwashirikisha vijana kikamilifu katika ujenzi wa uchumi wa Taifa. 

“Serikali inataka vijana wawe sehemu halisi ya maendeleo na kushiriki kikamilifu na si watazamaji tu.”Ameongeza.

Aidha ameeleza kuwa kabla ya mchakato wa kuwapata washindi watatu, maombi zaidi ya 7000 yalipokelewa na kuchujwa hadi kufikia vijana 100 waliopatiwa mafunzo na kusisitiza kuwa Serikali itaunda mfumo wa kuwafuatilia baada ya shindano.

“Ili mawazo yao yasibaki kwenye makabati wataunganishwa na fursa, taasisi za fedha na viongozi wa taasisi mbalimbali ili mawazo yaweze kuleta tija kwa jamii na kusaidia vijana wengine.” Aliongeza.

Katika matokeo yaliyotangazwa kwenye fainali ya shindano hilo, Jofrey Sanga ameibuka mshindi wa kwanza na kujishindia shilingi milioni 50, Jacob Fabian ameshika nafasi ya pili na kutwaa zawadi ya shilingi milioni 30, huku Robert Malonga akimalıza katika nafasi ya tatu na kujinyakulia kitita cha shilingi milioni 20 kupitia mawazo ya kibunifu yanayoweza kuchangia mandeleo ya Taifa katika kujenga uchumi imara, shindani na unaojumuisha ubunifu kama nguzo muhimu ya maendeleo endelevu.

Waziri Mkuu wa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Mwigulu Nchemba akizungumza katika hafla ya kuwatambua na kutoa zawadi kwa washindi wa shindano la Vijana Uchumi Challenge, Nchemba amesema Serikali itaendelea kutoa fursa kwa kundi hilo katika kuelekea Dira ya Maendeleo 2050.Leo jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - Maendeleo ya Vijana Dkt. Joel Nanauka akizungumza katika hafla hiyo na kusisitiza kuwa Serikali itaendelea kuwashirikisha vijana kikamilifu katika ujenzi wa uchumi wa Taifa. Leo jijini Dar es Salaam.


Matukio mbalimbali wakati wa Hafla ya kuwatambua na kutoa zawadi kwa washindi wa shindano la Vijana Uchumi Challenge, Leo jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Mbolea Tanzania (TFC), Samuel A. Mshote, amesema matumizi ya mbolea nchini yameendelea kuongezeka na kuchangia kupungua kwa changamoto kwa wakulima pamoja na kuimarika kwa usalama wa chakula nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), Julai 5, 2026, Mshote alisema hali ya uzalishaji wa chakula imeendelea kuimarika, ambapo kwa sasa Tanzania inajitosheleza kwa chakula kwa zaidi ya asilimia 124, na mafanikio hayo yanatokana na juhudi za Serikali katika kuhakikisha matumizi ya mbolea yanaongezeka nchini, hali iliyosaidia kuongeza tija katika sekta ya kilimo.

Mshote alisema matumizi ya mbolea yameongezeka kutoka takribani tani 360,000 kwa miaka mitatu iliyopita hadi zaidi ya tani milioni 1.2 kwa mwaka kwa mbolea aina mbalimbali zinazotumika na wakulima nchini, elimu kuhusu matumizi ya mbolea kwa wakulima imeendelea kuimarika, jambo ambalo linatarajiwa kuongeza zaidi tija katika uzalishaji wa mazao kadri muda unavyosonga mbele.

Aidha, alisema lengo la Serikali ni kuhakikisha matumizi ya mbolea yanafikia kilo 50 kwa hekta, ikiwa ni utekelezaji wa azimio la Umoja wa Afrika kwa nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara, lenye lengo la kuongeza uzalishaji wa kilimo, amebainisha kuwa ifikapo mwaka 2030, Tanzania inatarajia kufikia malengo ya uzalishaji yaliyowekwa kupitia azimio hilo ili kuimarisha zaidi sekta ya kilimo.

Kuhusu upatikanaji wa mbolea, alisema Kampuni ya Mbolea Tanzania (TFC) imeanza kutekeleza mipango mbalimbali ambapo tani 70,000 zimeingizwa nchini kwa ajili ya matumizi ya wakulima, pia tani 30,000 za mbolea za kupandia zinatarajiwa kupokelewa wiki ijayo, ambazo zitasambazwa kwa wakulima ili kuanza maandalizi ya msimu mpya wa kilimo.

Aidha, alieleza kuwa Serikali imeagiza tani 40,000 za mbolea aina ya Urea ambazo zinatarajiwa kupokelewa mwezi ujao kwa ajili ya kuingizwa sokoni na kusaidia wakulima katika hatua za kukuzia mazao.'



Shirika la Women Action Towards Economic Development (WATED) limesema limeshiriki katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) kwa kushirikiana na GIZ kama wafadhili ili kutoa matokeo ya mradi wa miezi minane uliokusanya simulizi na historia za manusura wa ukatili wa kijinsia wa kingono kutoka mikoa ya Tanga, Dodoma (Wilaya ya Bahi) na Dar es Salaam.

Akizungumza katika maonesho hayo, Maria Matui kutoka WATED amesema lengo la ukusanyaji wa simulizi hizo ni kuchochea mazungumzo katika jamii kuhusu changamoto za kijamii zinazochangia ukatili wa kijinsia na kuhamasisha hatua za kukabiliana nao.

Amesema kupitia mradi huo, wameweka mkazo katika kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu sheria, kanuni na taratibu zilizopo katika mifumo na sekta mbalimbali zinazoshughulikia masuala ya ukatili wa kijinsia, pamoja na namna manusura wanavyoweza kupata ulinzi, haki na huduma wanapokumbana na madhara ya ukatili huo.

Matui amesema huo ni mradi wa kwanza wa aina yake kufanyika nchini Tanzania, ambapo umefanikiwa kuwafikia manusura 26 kutoka mikoa hiyo mitatu na kubaini changamoto mbalimbali zinazohitaji kufanyiwa kazi.

Kwa mujibu wake, masuala yaliyojitokeza kupitia simulizi hizo yanahusu changamoto za kisheria, huduma za msaada wa kijamii, afya, elimu, pamoja na mila na desturi kandamizi,  ameeleza kuwa katika baadhi ya maeneo, bado zipo tamaduni zinazowafanya mabinti kutolewa kama njia ya kulipa madeni ya wazazi wao.

Aidha, amesisitiza kuwa Tanzania ina sheria na taratibu zilizowekwa kikatiba zinazolenga kulinda utu na haki za kila mwananchi, hivyo jamii inapaswa kuzifahamu na kuzitumia kuhakikisha manusura wa ukatili wa kijinsia wanapata ulinzi na haki stahiki.





Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Dkt. Eveline Munisi, amesema mahusiano mazuri kati ya wananchi, taasisi na wadau mbalimbali ni msingi muhimu wa maendeleo ya taifa.

Akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), Julai 5, 2026. Dkt. Munisi alisema Ofisi ya Waziri Mkuu inaendelea kushirikiana na taasisi za kijamii, taasisi za kidini, vyama vya siasa na asasi za kiraia ili kujenga umoja na mshikamano nchini.

Alisema jamii yenye mahusiano mazuri hujenga mazingira wezeshi ya maendeleo, hivyo akatoa wito kwa Watanzania kuendelea kudumisha ushirikiano, umoja na mshikamano kwa manufaa ya taifa.

Aidha, alisema Serikali inaendelea kuwekeza katika maendeleo ya ujuzi kwa vijana kupitia programu mbalimbali za mafunzo, akibainisha kuwa lengo ni kuhakikisha Tanzania inazalisha wataalamu wake na kuondoa utegemezi wa wataalamu kutoka nje ya nchi kwa miaka ijayo.

Dkt. Munisi pia aliwahimiza wananchi kutembelea banda la Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano) katika Maonesho ya Sabasaba ili kupata elimu na huduma mbalimbali zinazotolewa na taasisi zilizo chini ya ofisi hiyo.


 Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini kimesema kimejipanga kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwa kuzalisha watumishi wenye weledi kupitia ufundishaji, kufanya tafiti na kuandaa wataalamu watakaosaidia kuharakisha maendeleo ya taifa.

Akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya Sabasaba jijini Dar es Salaam Julai 4, 2026, Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Hozen Mayaya, alisema chuo kinaendelea kuandaa rasilimali watu wenye ujuzi na uwezo wa kufanya kazi katika taasisi za serikali na sekta binafsi.

Alisema ili kufanikisha Dira ya Taifa 2050 ni lazima taifa liwe na rasilimali watu wenye uwezo wa kufanya kazi kwa ufanisi, huku akibainisha kuwa asilimia 70 ya mchango katika utekelezaji wa Dira hiyo unatarajiwa kutoka katika sekta binafsi.

Profesa Mayaya alisema chuo kitaendelea kufanya tafiti zitakazosaidia kutatua changamoto zitakazojitokeza wakati wa utekelezaji wa Dira hiyo kwa kutoa suluhisho kwa taasisi mbalimbali.

Aidha, alieleza kuwa chuo bado kinapokea wanafunzi wanaotaka kujiunga na kozi mbalimbali kuanzia ngazi ya cheti hadi shahada, amebainisha kuwa idadi ya wanafunzi imeongezeka kutoka chini ya 30 wakati wa kuanzishwa kwa chuo hadi zaidi ya elfu 15,000 kwa sasa.

Amesema ongezeko hilo linaonyesha imani ya wananchi kutokana na ubora wa elimu na maboresho ya miundombinu yaliyowekwa na serikali, huku akitumia jukwaa hilo kuwakaribisha wazazi, walezi wa wanafunzi waliohitimu kuweza kuona kuwa ni sehemu sahihi ya kuwapeleka Watoto wao kupata elimu na ujuzi.

Amesema wahitimu wengi wameajiriwa sekta za umma na binafsi, baadhi wamejiajiri  pamoja na kuwaajiri wengine, ambapo kwasasa Makao Makuu ya chuo hicho yapo Jijini Dodoma na Kampasi ndogo ipo Jijini Mwanza huku matarajio Yao nikuongeza Kampasi katika maeneo mengine nchini ikiwemo Daresalam.






Na Mwandishi Wetu, Michuzi TV

BODI ya Utalii Tanzania (TTB), imesema moja ya jukumu lake kubwa ni kutangaza utalii wa Tanzania ndani na nje ya nchi, hivyo Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba)yanayoendelea ni jukwaa muhimu la kuendelea kutangaza utalii wetu.

Aidha imesema kupitia maonesho hayo ya Sabasaba pia yamekuwa jukwaa muhimu la kuhamasisha utalii wa ndani, kutangaza vivutio vya utalii na kuwaandaa wadau kunufaika na fursa mbalimbali ikiwemo mashindano ya AFCON yanayotarajiwa kufanyika mwaka ujao.

Akizungumza katika maonesho hayo Naomi Mbilinyi ambaye ni Ofisa Utalii Mwandamizi wa Bodi ya Utalii Tanzania amesema kupitia banda la TTB, wananchi wanapata taarifa kuhusu fursa zilizopo katika sekta ya utalii, ikiwemo namna ya kuanzisha kampuni za utalii, kushiriki maonesho ya kimataifa na kutembelea vivutio mbalimbali vilivyopo nchini.

“TTB pia inatumia maonesho hayo kutangaza Swahili International Tourism Expo, yatakayofanyika mwezi Oktoba, ambapo wadau wanapata fursa ya kujisajili kama waoneshaji, wadhamini na washiriki wa maonesho hayo ya kimataifa.”

Ameongeza pia bodi hiyo inaendelea kujenga mfumo wa kidijitali utakaowezesha wadau wa utalii kusajili taarifa za biashara zao ili kutangaza huduma na vivutio vyao kwa urahisi katika masoko ya ndani na nje ya Tanzania.

Kwa mujibu wa Mbilinyi, banda la TTB pia limetenga eneo maalum la kutoa elimu kuhusu fursa zitakazotokana na mashindano ya AFCON, likiwaelimisha watoa huduma za malazi, usafiri na sekta nyingine jinsi ya kujiandaa kupokea wageni wengi watakaoingia nchini wakati wa mashindano hayo.

Amesema wageni wengi wanaotembelea banda hilo, hususan wakazi wa Dar es Salaam, huonyesha hamu ya kujifunza kuhusu maeneo ya utalii yaliyo karibu nao, ikiwemo fukwe, maeneo ya kihistoria, makumbusho na vivutio vingine vinavyoweza kutembelewa kwa safari za siku moja (city tour).

Pia amesema wananchi wengi huulizia gharama za kutembelea hifadhi za taifa na maeneo mengine ya utalii, ambapo TTB hushirikiana na taasisi mbalimbali za sekta hiyo kuwapa taarifa sahihi na kuwaelekeza kwenye mabanda husika.

Ametoa wito kwa wananchi, Mbilinyi aliwahimiza kutembelea banda la TTB katika Maonesho ya Sabasaba ili kupata taarifa mbalimbali ambazo si rahisi kuzipata sehemu nyingine, ikiwemo usajili wa mifumo ya kidijitali, taarifa kuhusu Swahili International Tourism Expo na maandalizi ya AFCON.

“Maonesho hayo yanatoa nafasi ya wananchi kuzungumza moja kwa moja na wataalamu wa utalii, kuuliza maswali, kutoa maoni na kupata mwongozo kuhusu fursa zilizopo katika sekta ya utalii nchini.”









 Na Benny Mwaipaja, Banjul, Gambia


Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amewasili Banjul nchini Gambia kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa African Caucus wa 2026, utakaofanyika kuanzia jumatatu tarehe 6 Julai, 2026, unatarajiwa kuwa tukio muhimu litakalowakutanisha viongozi wa Afrika, watunga sera, wataalamu wa fedha, washirika wa maendeleo, na wawakilishi wa taasisi za kimataifa.

Mhe. Omar alipokelewa na Balozi wa Tanzania nchini Nigeria anayesimamia pia shughuli za kibalozi nchini Gambia, Mhe. Balozi Selestine Kakele, katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Banjul.

Mkutano huo utakaofanyika katika Kituo cha Mikutano cha SDJK, jijini Banjul, utatoa jukwaa kwa nchi za Afrika kujadili masuala muhimu ya uchumi na maendeleo yanayoikabili Bara la Afrika, pamoja na kuweka msimamo wa pamoja katika kushirikiana na taasisi kubwa za kifedha duniani.

African Caucus ni jukwaa linalowakutanisha magavana wa Afrika katika Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) na Kundi la Benki ya Dunia, ambalo huzisaidia nchi za Afrika kuzungumza kwa sauti moja kuhusu masuala kama usimamizi wa madeni, fedha za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, maendeleo ya miundombinu, kupunguza umasikini, ajira, biashara, na mageuzi ya kiuchumi.

Gambia kuandaa mkutano huo wa mwaka 2026 ni fursa kubwa kwa nchi hiyo kushiriki kikamilifu katika mijadala ya bara na kuonesha vipaumbele vyake vya maendeleo.

Mkutano huo unaweza kuleta faida nyingi ikiwemo kuongeza mwonekano wa nchi hiyo katika ngazi ya Afrika na kimataifa, kuvutia mijadala kuhusu uwekezaji, na kuimarisha ushirikiano kati ya Gambia, nchi nyingine za Afrika, na washirika wa maendeleo.

Pia unaweza kuonesha juhudi za Gambia katika maeneo kama mageuzi ya uchumi, utalii, kilimo, uwezeshaji wa vijana, mabadiliko ya kidijitali, na maendeleo endelevu.

Mkutano wa 2026 unaweza pia kujikita katika changamoto zinazozikabili nchi za Afrika, zikiwemo ongezeko la madeni, mabadiliko ya tabianchi, uhaba wa chakula, ukosefu wa ajira, na umuhimu wa kuimarisha ushirikiano wa kikanda.

Masuala haya ni muhimu hasa kwa nchi ndogo kama Gambia, ambapo athari za mabadiliko ya tabianchi, rasilimali chache, na utegemezi wa sekta chache zinaweza kuathiri maendeleo ya Taifa na upitia African Caucus, nchi zinaweza kubadilishana uzoefu na kupendekeza suluhisho za vitendo linaloendana na hali halisi ya Afrika.

Kuandaa mkutano huu pia kunaweza kuwa na matokeo chanya kwa biashara za ndani na sekta ya utalii. Hoteli, huduma za usafiri, migahawa, waandaaji wa matukio, na vikundi vya sanaa na utamaduni vinaweza kunufaika kutokana na uwepo wa wajumbe na wageni.

Tukio hili linaweza kuitangaza Gambia kama nchi yenye amani, ukarimu, na uwezo wa kuandaa mikutano ya kimataifa na shughuli za kidiplomasia.

Kwa ujumla, Mkutano wa African Caucus wa 2026 nchini Gambia ni tukio lenye umuhimu mkubwa kwa Gambia na Bara la Afrika kwa jumla kwani unatoa nafasi kwa viongozi wa Afrika kujadili vipaumbele vya pamoja, kuimarisha ushirikiano, na kutetea haki zaidi kutoka kwa taasisi za kifedha duniani.

Kwa Gambia, huu ni wakati wa kuonesha uongozi, kutangaza malengo yake ya maendeleo, na kujitambulisha kama mshirika muhimu katika mustakabali wa uchumi wa Afrika.


Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb)(kushoto), akisalimia na Balozi wa Tanzania nchini Nigeria anayesimamia pia shughuli za kibalozi nchini Gambia, Mhe. Balozi Selestine Kakele, wakati alipowasili jijini Banjul nchini Gambia kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa African Caucus wa 2026, utakaofanyika kuanzia jumatatu tarehe 6 Julai, 2026, unatarajiwa kuwa tukio muhimu litakalowakutanisha viongozi wa Afrika, watunga sera, wataalamu wa fedha, washirika wa maendeleo, na wawakilishi wa taasisi za kimataifa.


Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb)(kushoto), akiteta jambo na Balozi wa Tanzania nchini Nigeria anayesimamia pia shughuli za kibalozi nchini Gambia, Mhe. Balozi Selestine Kakele, wakati alipowasili jijini Banjul nchini Gambia kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa African Caucus wa 2026, utakaofanyika kuanzia jumatatu tarehe 6 Julai, 2026, unatarajiwa kuwa tukio muhimu litakalowakutanisha viongozi wa Afrika, watunga sera, wataalamu wa fedha, washirika wa maendeleo, na wawakilishi wa taasisi za kimataifa.

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb)(kulia), akiwa katika picha na Balozi wa Tanzania nchini Nigeria anayesimamia pia shughuli za kibalozi nchini Gambia, Mhe. Balozi Selestine Kakele, wakati alipowasili jijini Banjul nchini Gambia kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa African Caucus wa 2026, utakaofanyika kuanzia jumatatu tarehe 6 Julai, 2026, unatarajiwa kuwa tukio muhimu litakalowakutanisha viongozi wa Afrika, watunga sera, wataalamu wa fedha, washirika wa maendeleo, na wawakilishi wa taasisi za kimataifa.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini,WF, Banjul, Gambia)
Ecobank Tanzania imeendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu huduma mbalimbali za kifedha kupitia ushiriki wake katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Sabasaba yanayoendelea katika Viwanja vya Julius Nyerere, Dar es Salaam, ambapo banda lake linapatikana katika Kijiji cha Bima kinachosimamiwa na Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA).

Akizungumza katika maonesho hayo, mwakilishi wa Ecobank amesema benki hiyo inatoa huduma mbalimbali za kifedha zinazolenga kukidhi mahitaji ya watu binafsi, wafanyabiashara na taasisi, huku ikiwapa wateja suluhisho la huduma za benki kwa urahisi na ufanisi.

Ameeleza kuwa miongoni mwa huduma zinazotolewa ni "Saving Account", ambayo haina makato ya kila mwezi na humruhusu mteja kuweka na kutoa fedha wakati wowote kulingana na mahitaji yake.

Aidha, amesema Ecobank inatoa "Current Account", inayomwezesha mteja kupata huduma ya "Overdraft", inayomruhusu kutumia fedha zinazozidi salio lililopo kwenye akaunti kwa muda wa hadi siku 14, kwa kuzingatia masharti ya benki.

Vilevile, benki hiyo inatoa mikopo ya muda mfupi na muda mrefu kwa makundi mbalimbali yakiwemo watumishi wa umma, wafanyabiashara na watu binafsi, pamoja na mikopo ya ujenzi na ununuzi wa nyumba.

Mbali na huduma za benki, Ecobank pia inatoa huduma mbalimbali za bima zikiwemo bima ya nyumba, magari na afya, kwa kushirikiana na wadau wake wa sekta ya bima, ikiwa ni sehemu ya kuwapatia wateja huduma za kifedha zilizounganishwa katika eneo moja.

Ecobank imewahimiza wananchi wanaotembelea Maonesho ya Sabasaba kutembelea banda lake lililopo Kijiji cha Bima (TIRA) ili kupata elimu zaidi kuhusu huduma za benki na bima, kufungua akaunti, kupata ushauri wa kifedha na kufahamu fursa mbalimbali zinazotolewa na benki hiyo.
Mkuu wa kitengo cha Wateja Binafsi na Biashara kutoka Ecobank Tanzania, Joyce Ndyetabura akimsikiliza mfanyakazi wa Ecobank Tanzania walipokuwa wanatoa huduma katika maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Sabasaba yanayoendelea jijini Dar es Salaam ambapo banda lake linapatikana katika Kijiji cha Bima kinachosimamiwa na Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA).
Watumishi wa Ecobank Tanzania wakitoa elimu katika maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Sabasaba yanayoendelea jijini Dar es Salaam.

Mkuu wa Kitengo cha Biashara kwa Wateja Wakubwa (Commercial Banking) Joyce Ndyetabura akiwa kwenye picha ya pamamo na watumishi wa Ecobank Tanzania katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Sabasaba yanayoendelea katika Viwanja vya Julius Nyerere, Dar es Salaam, ambapo banda lake linapatikana katika Kijiji cha Bima kinachosimamiwa na Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA).
NA FARIDA MANGUBE
WAZIRI  wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mheshimiwa Prof. Riziki Silas Shemdoe (Mb), ameipongeza Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) kwa kazi kubwa ya kuunganisha mawasiliano ya barabara kutoka kijiji hadi kijiji na wilaya hadi wilaya, akisema kuwa jukumu hilo ni gumu na linahitaji weledi, uzalendo na utendaji wa hali ya juu.

Prof. Shemdoe alitoa pongezi hizo alipokagua maendeleo ya ujenzi wa Daraja la Isago lenye urefu wa mita 42.6 katika Kata ya Mngeta, Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba, mkoani Morogoro, akiwa katika ziara ya kikazi ya tarehe 2 hadi 6 Julai 2026 Mkoani humo.

Akizungumza mara baada ya kupokea taarifa ya mradi iliyosomwa na Meneja wa TARURA Mkoa wa Morogoro, Mhandisi Emmanuel Ndyamukama, Waziri Shemdoe amesema Serikali inaendelea kuwekeza katika miundombinu ya barabara na madaraja ili kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kuboresha maisha ya wananchi.

"TARURA mmefanya kazi kubwa sana ya kuunganisha wananchi kupitia mtandao wa barabara vijijini. Kazi hii si rahisi; inahitaji utaalamu, kujituma na uwezo wa kufanya kazi katika mazingira magumu. Serikali inatambua mchango wenu na inawapongeza kwa juhudi zenu za kuhakikisha wananchi wanapata huduma za usafiri na usafirishaji wakati wote," amesema Prof. Shemdoe.

Aidha, Waziri huyo aliwataka mkandarasi na mshauri wa mradi kuongeza kasi ya utekelezaji ili mradi ukamilike kwa wakati na kwa viwango vinavyokubalika, huku akisisitiza matumizi sahihi ya fedha za umma na ubora wa kazi zinazotekelezwa.

Mhandisi Emmanuel Ndyamukama ni Meneja wa TARURA Mkoa wa Morogoro, amesema mradi wa ujenzi wa Daraja la Isago ni miongoni mwa miradi ya kimkakati inayofadhiliwa na Benki ya Dunia kupitia Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa lengo la kuboresha miundombinu katika maeneo ya uzalishaji vijijini, kuimarisha uchumi na kuongeza uwezo wa kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi pamoja na majanga ya asili.

Mkataba wa ujenzi wa daraja hilo ulisainiwa tarehe 15 Desemba 2025 kati ya Katibu Mkuu wa TAMISEMI na kampuni ya ENGISOFT Company Limited kwa thamani ya shilingi bilioni 1.738 (bila kodi), huku usimamizi wa mradi ukifanywa na kampuni za LUPTAN Consults Ltd kwa kushirikiana na Afro Base & ORU Consults.

Mradi huo unahusisha ujenzi wa daraja lenye urefu wa mita 42.6, barabara za maingilio zenye urefu wa mita 300, ujenzi wa makalvati mawili pamoja na kuinua tuta katika eneo la mradi.

Utekelezaji ulianza rasmi Januari 1, 2026 na unatarajiwa kukamilika Agosti 30, 2026. Hadi sasa, utekelezaji umefikia asilimia 20, huku mkandarasi akiwa amelipwa malipo ya awali yenye jumla ya shilingi milioni 260.7.

Daraja la Isago linatarajiwa kuunganisha kwa urahisi maeneo ya kilimo kati ya Mngeta na Isago, kurahisisha usafiri wa wananchi kufikia huduma muhimu za elimu, afya na biashara, pamoja na kupunguza athari za mafuriko ambazo zimekuwa zikisababisha usumbufu mkubwa kwa wakazi wa eneo hilo.

Mhandisi Ndyamukama imesema mradi umekumbwa na changamoto ya kuchelewa kwa utekelezaji kutokana na mvua kubwa za msimu zilizonyesha mkoani Morogoro na kuathiri baadhi ya shughuli za ujenzi.

Kwa upande wao Watumiaji wa Barabara na wakazi wa Kata ya Mngeta akiwemo Rajabu Sudi amesema kukamilika kwa daraja hilo kutarahisisha usafirishaji wa mazao ya kilimo kwenda sokoni, kupunguza gharama za usafiri na kuongeza fursa za biashara na uwekezaji katika eneo hilo.

Nae Elizabeth Sanga mkazi wa Kijiji cha Isago amesema kwa miaka mingi walikuwa wakipata shida kuvuka eneo hilo kipindi cha mafuriko, hali iliyosababisha wanafunzi kukosa masomo, wagonjwa kushindwa kufika kwenye vituo vya afya kwa wakati na wafanyabiashara kuchelewa kufikisha bidhaa zao sokoni.

Amesema ujenzi wa daraja hilo ni suluhisho la kudumu ambalo litabadilisha maisha ya wakazi wa eneo hilo.





Na Mwandishi Wetu
SHIRIKA la Mawasiliano Tanzania (TTCL) limesema litaendelea kuimarisha huduma za mawasiliano nchini kwa kuendeleza matumizi ya Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano, kupanua huduma za kidijitali na kuwekeza katika teknolojia za kisasa ili kuongeza mchango wake katika ukuaji wa uchumi wa kidijitali.

Mkurugenzi Mkuu wa TTCL, Moremi Marwa, amesema mafanikio yanayoendelea kupatikana ndani ya shirika hilo yametokana na maboresho ya kiutendaji na kibiashara yaliyofanyika katika kipindi cha hivi karibuni, hatua ambayo imewezesha TTCL kuongeza mapato, kupata faida na kuboresha huduma kwa wananchi.

Akizungumza katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba), Marwa alisema TTCL imeutumia mkutano huo kama jukwaa la kuonesha teknolojia na huduma mbalimbali zinazochochea maendeleo ya uchumi wa kidijitali kupitia Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano.

Alisema miongoni mwa huduma zinazotolewa ni intaneti ya kasi ya juu ya Supersonic Speed, kituo cha FTTX Experience Center kinachowawezesha wananchi kujionea matumizi ya teknolojia ya nyumba janja (Smart Home), pamoja na huduma za Cloud Computing kupitia Kituo cha Taifa cha Kuhifadhi Data (National ICT Data Centre – NIDC).

Marwa alifafanua kuwa huduma za Cloud Computing zinazotolewa kupitia NIDC zinawapa wateja fursa ya kuhifadhi taarifa na mifumo yao kwa usalama wa hali ya juu bila kulazimika kuwekeza gharama kubwa katika miundombinu ya kuhifadhi data, jambo linalosaidia kuongeza ufanisi wa shughuli za taasisi na biashara.

Akizungumzia utendaji wa shirika hilo, alisema TTCL imepata faida ya takribani shilingi bilioni 23 katika mwaka wa fedha 2024/2025, huku matokeo ya awali ya mwaka wa fedha 2025/2026 yakionyesha kuongezeka kwa mapato, faida na idadi ya wateja wanaotumia huduma za shirika hilo.

Alisema mafanikio hayo yametokana na utekelezaji wa maboresho ya kimkakati yaliyofanywa kufuatia maelekezo ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha TTCL linaendeshwa kwa misingi ya kibiashara, linaongeza mapato na kuondokana na utegemezi wa hasara.

Marwa alisisitiza kuwa TTCL itaendelea kuwekeza katika teknolojia za kisasa na kuboresha miundombinu ya mawasiliano ili kuhakikisha Watanzania wanapata huduma bora, salama na za uhakika zinazochangia maendeleo ya uchumi wa kidijitali na Taifa kwa ujumla.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
KAMPUNI ya GF Group imeandika historia kwa kutwaa tuzo ya Banda Bora kwa Ujumla katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) kwa mwaka wa pili mfululizo, mafanikio ambayo yameelezwa kuwa ni matokeo ya ubunifu, nidhamu, mshikamano na kujituma kwa wafanyakazi wake.

Akizungumza na Wafanyakazi pamoja na Wadau Mbalimbali Mkurugenzi Mtendaji wa GF Group Imran Karmali amesema tuzo walioipata ni ushindi ulipatikana sio kwa bahati mbaya bali ni matokeo ya uthibitisho wa dhamira ya kampuni ya kuwa kinara katika sekta ya magari na viwanda nchini Tanzania.

Amesema kuwa miaka 19 tangu kuanzishwa kwake GF Group kutoka kuwa na maono ya kawaida hadi kuwa miongoni mwa makundi makubwa ya biashara ya magari nchini, ikiwa inawakilisha chapa mbalimbali za kimataifa, kuunganisha magari hapa nchini, kuwekeza katika maendeleo ya watu, kuzalisha ajira na kuchangia ukuaji wa sekta ya viwanda.

Ilielezwa kuwa kampuni hiyo haijikiti tena katika uuzaji wa magari pekee, bali sasa inaunganisha magari nchini, inaleta teknolojia mpya, inajenga uwezo wa wataalamu wa ndani na kuwekeza katika uzalishaji unaoifanya Tanzania kuwa kitovu cha maendeleo ya sekta ya magari.

Aidha, GF Group imetangaza hatua nyingine muhimu ya kihistoria kwa kuanza kuingiza sokoni bidhaa zinazobeba chapa yake yenyewe ya GF, hatua ambayo inaonyesha uwezo wa kampuni hiyo kutengeneza na kukuza bidhaa za Kitanzania zenye ubora wa kimataifa.

Kwa mujibu wa kampuni hiyo, lengo si kutengeneza magari kwa ajili ya Tanzania pekee, bali kuzalisha bidhaa zinazobuniwa kwa mahitaji ya Afrika, kutengenezwa nchini Tanzania na kuaminiwa katika duniani.

Karmali amesema tuzo hiyo haihusu uzuri wa banda pekee, bali ni ishara ya kutambuliwa kwa ubunifu, weledi, maono na uwezo wa kutekeleza mipango mikubwa kwa mafanikio.

Hata hivyo amesema wafanyakazi wa GF Group walihimizwa kuendelea kuwa mabalozi wa kampuni kwa kuhakikisha kila huduma wanayotoa, kila uamuzi wanaoufanya na kila gari wanalolizalisha linaendelea kujenga sifa ya kampuni hiyo ndani na nje ya Tanzania.

Amesema GF Group katika sekta ya magari duniani inaendelea kubadilika kutokana na ujio wa magari ya umeme na teknolojia za kidijitali, hivyo kampuni imejipanga kuwa sehemu ya kuunda mustakabali huo badala ya kuusubiri.

Uongozi huo ulisisitiza kuwa ushindi wa mwaka huu ni hatua moja tu katika safari ndefu ya kujenga kampuni ya Kitanzania inayoweza kushindana na kampuni bora barani Afrika kwa ubora wa bidhaa, ubunifu, uadilifu, uzalishaji wa kisasa na uwezo wa kuunda fursa kwa Watanzania.

Karmali amesema wafanyakazi wote wana mchango wao katika mafanikio hayo huku akiahidi kuendelea kuinua viwango vya utendaji na kuacha urithi utakaowanufaisha vizazi vijavyo.




Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
JUMLA ya wananchi 1,940 wamepata huduma za uchunguzi wa macho na ushauri wa kitabibu bila malipo katika Banda la MIXX kwenye Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika banda hilo, Mtaalamu wa Macho na Huduma kwa Jamii kutoka Taasisi ya Bilal Muslim, Patrick Martine, alisema huduma hiyo imewezesha wananchi kupimwa afya ya macho na kupatiwa miwani bure kulingana na mahitaji yao.

Alisema kati ya wananchi waliopimwa, watu 41 walibainika kuwa na tatizo la mtoto wa jicho na wataendelea kupatiwa matibabu kupitia Taasisi ya Bilal Muslim.

Martine alisema ushirikiano kati ya MIXX na Taasisi ya Bilal Muslim umewezesha wananchi wengi kupata huduma ambazo kwa kawaida zingehitaji gharama kubwa, huku akiwataka wananchi kutumia fursa hiyo kabla ya maonesho kumalizika.

Aidha, alieleza kuwa baadhi ya changamoto za macho zinazoongezeka kwa sasa zinachangiwa na matumizi ya muda mrefu ya vifaa vya kielektroniki kama televisheni na simu, pamoja na sababu nyingine za kiafya zinazohitaji uchunguzi wa mapema.

Kwa upande wake, Meneja wa Banda la MIXX, Omega Mwakifuna, alisema utoaji wa huduma za macho ni sehemu ya mkakati wa kampuni wa kurudisha kwa jamii kwa kuwasaidia wananchi kupata huduma muhimu za afya bila gharama.

Alisema MIXX itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha wananchi wote watakaotembelea banda hilo na kuhitaji huduma za macho wanapata fursa ya kupimwa na kupatiwa ushauri wa kitaalamu.

Baadhi ya wananchi walionufaika na huduma hiyo wameipongeza MIXX kwa kuwaletea huduma karibu yao.

Mkazi wa Kijichi, Cecilia Kapituka, alisema amepimwa macho na kupatiwa miwani miwili bure, jambo ambalo limemsaidia kupata suluhisho la tatizo lililokuwa likimsumbua kwa muda mrefu.

Naye mkazi wa Mabibo, Daud Bernad, alisema amefurahishwa na huduma hiyo baada ya kupimwa na kupatiwa miwani bila malipo, huku akiwahamasisha wananchi wengine kutembelea Banda la MIXX katika Maonesho ya Sabasaba ili kunufaika na huduma hiyo muhimu.






Top News