WANANCHI wa Kitongoji cha Shuleni, Kijiji cha Holili Vijijini wilayani Rombo mkoani Kilimanjaro, wamelalamikia athari za maji ya mvua yaliyoelekezwa kwenye makazi yao kufuatia uchimbaji wa mitaro uliofanywa na Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA). 

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na waandishi wa habari jana, wananchi hao  wamesema hali hiyo imeanza kuleta madhara tangu kuanza kwa mvua za masika.

Akizungumza kwa niaba ya wananchi, Ibrahim Tarimo amesema mitaro hiyo imeelekeza maji moja kwa moja kwenye mashamba na makazi, hali iliyosababisha baadhi ya nyumba kuingiliwa na maji na hata ukuta wa uzio wa  nyumba ya mkazi mmoja kuanguka kufuatia mvua zinazonyesha hali ambayo inaleta hofu kubwa hasa kwa watoto wanaobaki nyumbani peke yao wakati wa mchana.

Kwa upande wake, Julius Lazaro amesema changamoto hiyo ilianza tangu mwishoni mwa mwaka 2025 baada ya TARURA kutengeneza barabara na kuelekeza mitaro kwenye makazi ya wananchi, hali inayowafanya wananchi kuishi kwa hofu hasa nyakati za usiku mvua zinaponyesha.

Amesema kuwa baada ya madhara hayo, waliwasilisha malalamiko yao kwa TARURA ambao walifika eneo la tukio na kuahidi kulifanyia kazi, lakini hadi sasa bado  hatua hazijachukuliwa.

“Barabara imetengenezwa vizuri, lakini changamoto ni haya maji yanayokuja moja kwa moja kwenye makazi yetu,” amesema.

Kwa upande wake, Medilaster Tarimo amesema maji hayo yameharibu mashamba na kuingia ndani ya nyumba yake, na kwamba anahofia madhara zaidi endapo mvua zitaendelea kunyesha bila hatua kuchukuliwa.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Holili Vijijini, Peter Mandu alisema tayari taarifa za tatizo hilo zimefikishwa kwa TARURA pamoja na kwa mkurugenzi wa halmashauri, na kwamba mhandisi alishafika eneo hilo kujionea hali halisi. 

Ameongeza kuwa ni muhimu hatua za haraka zichukuliwe ili kuelekeza maji kwenye makorongo na kuepusha madhara zaidi.

Akizungumzia Suala hilo, Meneja wa TARURA Wilaya ya Rombo, Rickson Lema amesema tayari wamefika eneo husika na kufanya ukaguzi kwa kushirikiana na wananchi na kwamba upo mpango wa kuchepusha maji hayo, lakini unahitaji makubaliano kutoka kwa wananchi hasa wamiliki wa mashamba yatakayopitishwa mtaro mpya.

“Tulishauriana na wananchi kuhusu uwezekano wa kuelekeza maji kwenye korongo. Tunawasubiri wakubaliane kupitia serikali ya kijiji ili tuanze utekelezaji wa mradi huo,” amesema Lema.

Na: Dk. Reubeni Lumbagala

Maji ni miongoni mwa huduma muhimu ya kijamii. Maji ni huduma ambayo kila mtu anahitaji tena kila siku. Utahitaji maji kwa kuoga, kupikia, kufulia, kupigia mswaki, kunyweshea mifugo, kumwagilia maua au bustani. Mambo yanayohitaji maji ni mengi. Maji haya yanapaswa kusambazwa kutoka katika vyanzo vyake mathalani mito, maziwa na mabwawa hadi katika makazi ya watu ili yaweze kutumiwa. Wananchi wanataka maji yawafikie katika makazi yao, hiyo ndiyo kiu na hitaji lao.

Waziri wa Maji, Jumaa Aweso anatoa ushuhuda wa hali ya maji iliyokuwa hapo nyuma. "Kitendo cha wananchi wa maeneo mbalimbali nchini kukosa maji kuliifanya Wizara ya Maji kuwa ni Wizara ya kero na lawama, lakini kwa kazi kubwa alizofanya Rais Dk. Samia, leo Wizara imekuwa faraja kwa wananchi," anasema Aweso. Maneno  ya Waziri Aweso yanatokana na ukweli kuwa katika maeneo mengi nchini, wananchi walikabiliwa na shida ya maji, hivyo walikuwa na lawama nyingi kwa Wizara ya Maji kwani ndiyo yenye dhamana ya kuhakikisha huduma ya maji inawafikia wananchi kule walipo, hivyo Wizara ya Maji haikuwa na namna ya kukwepa lawama hizo.

Kutokana na utashi wa kisiasa uliopo wa serikali wa kutatua kero za wananchi ikiwemo kero ya ukosefu wa maji, serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan imechukua hatua stahili na madhubuti kuhakikisha Wizara ya Maji inakuwa faraja kwa wananchi kwa kuwafikishia huduma ya maji na hivyo maji kuchangia maendeleo ya sekta nyingine ili kwa pamoja kasi ya maendeleo iweze kuongezeka. 

Waziri Aweso anakiri Rais Dk. Samia ameleta mageuzi makubwa ya kimaendeleo kwani miradi ya maji iliyokuwa imekwama sasa inafanya kazi na maji yanatoka. Ni ukweli mtupu kuwa Rais Dk. Samia anaumizwa na shida ya wananchi kutembea umbali mrefu kwenda kutafuta maji ambayo wakati mwingine hayana uhakika wa kuyapata. Muda wa kufanya shughuli za kijamii na kiuchumi wananchi inabidi wautumie kutafuta maji  kwa matumizi mbalimbali kama ya kupikia, kufulia na kuogea.

Ndoa zilikuwa zipo njia panda. Wanandoa wanagombana kwa sababu mke amechelewa kurudi nyumbani kutoka kisimani, bombani au mtoni kuchota maji. Watoto wanachelewa kwenda shule kutokana na kutafuta maji. Rais Dk. Samia amefanya kazi kubwa kwa kuongeza bajeti ya Wizara ya Maji kutoka shilingi  bilioni 680.3 mwaka wa fedha 2021/2022 hadi shilingi trilioni 1.01 mwaka wa fedha 2025/2026. Mapinduzi haya makubwa yamefanikisha kuongezeka kasi ya usambazaji maji kwa wananchi hali inayoleta faraja badala ya lawama.

Rais Dk. Samia amefanikisha uzinduzi wa miradi ya maji kuwa endelevu badala ya miradi hiyo kutoa maji pale tu wanapokuja viongozi kukagua na kuzindua. Uendelevu wa miradi ya maji inatoa uhakika wa wananchi kupata maji safi, salama na yenye kutosheleza. Waziri Aweso anasisitiza Rais Dk. Samia kuwa kinara wa maji kwani miradi iliyokuwa imekwama tangu miaka ya 1970, sasa imekamilika na inatoa maji. Wizara ya Maji imekuwa faraja kwa wananchi kutokana na fedha za miradi kutolewa kwa wakati kugharamia miradi hiyo. Jambo la kufurahisha hapa ni kwamba, fedha nyingi za miradi ya maji ni mapato ya ndani (own sources) badala ya kutegemea misaada ya wahisani. 

Kwa mujibu wa Waziri Aweso, katika kipindi cha miaka minne ya uongozi wa Rais Dk. Samia, zaidi ya shilingi trilioni tatu zimetolewa kugharamia miradi ya maji, jambo linaloongeza kasi ya usambazaji maji kwa wananchi. Katika kuendeleza tabasamu kwa wananchi, Wizara ya Maji inatekeleza mpango mkakati wa ujenzi wa Gridi ya Taifa ya Maji ili kuhakikisha maji yanakuwa ya kuhakika kwa matumizi mbalimbali ya kimaendeleo.

Katika Wiki ya Maji iliyozinduliwa Machi 16 hadi 22, 2026, Wizara ya Maji ina kila sababu ya kutembea kifuambele kutokana na mafanikio makubwa yaliyopatikana likiwemo suala la upatikanaji wa maji kufikia asilimia 92.5 maeneo ya mijini na asilimia 85.2 maeneo ya vijijini. Kazi nzuri zimefanyika. Kwa maeneo ambayo maji hayajafika, dhamira ya serikali ni ile ile kuwafikishia wananchi wake wote maji safi, hivyo kazi ya kufikisha maji kwa wananchi wote inaendelea tena kwa kasi na viwango vikubwa.

Maoni: 0620 800 462.







Balozi wa Tanzania nchini Zimbabwe, Kamishna wa Polisi (CP) Suzan Kaganda, ametembelea ofisi za Mamlaka ya Bandari ya Tanzania (TPA) zilizopo mjini Harare na kufanya mazungumzo na Mwakilishi wa TPA nchini humo, Bi. Kulthum Boma kuhusu namna ya kuimarisha huduma na kuongeza ufanisi katika usafirishaji wa mizigo kupitia bandari za Tanzania.

Ziara ya Mheshimiwa Balozi Kaganda ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Diplomasia ya Uchumi, ikiwa na lengo la kutambua na kuendeleza mchango wa TPA katika usafirishaji wa mizigo kutoka bandari za Tanzania kwenda nchi za Kusini mwa Afrika, ikiwemo Zimbabwe.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Bi. Kulthum Boma alieleza kuwa ofisi hiyo, yenye jukumu la masoko na huduma kwa wateja, imekuwa na mchango chanya katika kuongeza shehena ya mizigo inayoingia Zimbabwe kupitia bandari za Tanzania tangu kufunguliwa kwake rasmi mwaka 2023.

Kwa upande wake, Mheshimiwa Balozi Kaganda amepongeza mafanikio hayo na kusisitiza umuhimu wa ushirikiano wa karibu kati ya ofisi ya TPA na Ubalozi.

Vilevile ameshauri kuandaliwa kwa mikutano na wadau pamoja na wafanyabiashara nchini Zimbabwe ili kutumia majukwaa hayo kutoa elimu na kuongeza uelewa kuhusu matumizi ya bandari za Tanzania.

Hatua hiyo inatarajiwa kuchangia zaidi katika kukuza biashara na kuongeza pato la Taifa.






Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amewasihi Viongozi wa Dini kuendelea kuwekeza katika kufundisha maadili mema kwa kizazi cha sasa ili kuwa na Taifa zuri baadaye.

Makamu wa Rais amesema hayo wakati aliposhiriki Futari iliyoandaliwa na Jumuiya ya Maridhiano na Amani Tanzania (JMAT) iliyohusisha Viongozi wa Dini na Wadau wa Amani nchini, iliyofanyika Jijini Dar es Salaam tarehe 19 Machi 2026. Amesema ni vema kutoa kipaumbele cha pekee katika eneo la maadili kwa kuwa kuharibika kwa malezi ya sasa ni kuharibu kizazi kijacho.

Amesema kumekua na changamoto katika maadili na makuzi ya watoto, hivyo Viongozi wa Dini watakapoweka kipaumbele katika kufundisha maadili kwa waumini watakuwa wametoa mchango mkubwa kwa jamii na Taifa kwa ujumla.

Makamu wa Rais, ameipongeza Jumuiya ya Maridhiano na Amani (JMAT) kwa kazi kubwa waliyofanya ya kuimarisha mahusiano ya dini mbalimbali hapa nchini. Amesema Serikali inatambua na kuthamini kazi inayofanya Jumuiya hiyo ikiwa ni pamoja na kuelimisha wajibu wa viongozi wa dini na wajibu waumini katika kutambua nafasi zao kuleta amani nchini.

Makamu wa Rais amesema Tanzania inajivunia kuwa nchi ambayo wananchi wake wana ushirikiano bila kujali dini zao, hivyo ni muhimu kuendelea kusimamia ushirikiano huo.

Aidha, amesema ni muhimu kuimarisha mambo yote yaliyofanywa kipindi cha toba yaani Mwezi Mtukufu wa Ramadhan na kwaresma na kuyaendeleza.

Futari hiyo imehudhuriwa na Viongozi wa dini mbalimbali, Mabalozi wanaowakilisha nchi zao Tanzania, Wakuu wa Taasisi mbalimbali, Wasanii, pamoja na wadau wa amani nchini.















 

Afisa Mlinda Mlaji Mwandamizi FCC Bi.Magdalena Hall,akitoa elimu kuhusu masuala ya kumlinda mlaji na mikataba ya walaji kwa wanafunzi wa Chuo Cha Ufundi Stadi VETA Kibaha ,ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Haki za Mlaji Duniani 2026.

....

KATIKA harakati za kuimarisha uelewa wa haki za walaji nchini, Tume ya Ushindani (FCC) leo Machi 19, 2026 imetoa elimu kwa wanachuo wa Chuo Cha Ufundi Stadi VETA Kibaha kuhusu masuala ya kumlinda mlaji na mikataba ya walaji, ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Haki za Mlaji Duniani 2026.

Elimu hiyo ilitolewa na FCC kwa lengo la kuwajengea uelewa wanachuo kuhusu haki zao wanapokuwa wanatumia bidhaa na huduma mbalimbali. Wanachuo walipata nafasi ya kujifunza mambo muhimu ambayo mara nyingi huyapuuzia katika maisha yao ya kila siku.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo,Afisa Mlinda Mlaji Mwandamizi FCC Bi.Magdalena Hall,amewaeleza wanachuo kuwa wengi wao huingia katika mikataba bila kusoma masharti yake, hali inayoweza kusababisha hasara au kunyimwa haki zao bila wao kutambua.

Amefafanua kuwa mikataba mingi hasa ya huduma za simu, mikopo na manunuzi ya mtandaoni huwa na vifungu vinavyohitaji umakini mkubwa kabla ya kukubaliwa. Hivyo aliwataka wanachuo kujenga utamaduni wa kusoma na kuelewa kila wanachosaini.

Aidha, amesema  kuwa mlaji ana haki ya kupata bidhaa bora, taarifa sahihi na huduma stahiki. Pale haki hizo zinapokiukwa, mlaji anatakiwa kuchukua hatua za kisheria au kuripoti kwa mamlaka husika.

"FCC imesisitiza kuwa elimu hii ni endelevu na inalenga kuwafikia makundi mbalimbali ya jamii ili kujenga taifa lenye walaji wenye uelewa na uwezo wa kufanya maamuzi sahihi."amesema Bi.Hall

Kwa ujumla, mafunzo hayo yamewajengea wanachuo uelewa mkubwa na kuwahamasisha kuwa mabalozi wa haki za walaji, huku yakichangia mafanikio ya maadhimisho ya Maadhimisho ya Siku ya Haki za Mlaji Duniani 2026.

Afisa Mlinda Mlaji Mwandamizi FCC Bi.Magdalena Hall,akitoa elimu kuhusu masuala ya kumlinda mlaji na mikataba ya walaji kwa wanafunzi wa Chuo Cha Ufundi Stadi VETA Kibaha ,ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Haki za Mlaji Duniani 2026.

Afisa Mlinda Mlaji Mwandamizi FCC Bi.Magdalena Hall,akitoa elimu kuhusu masuala ya kumlinda mlaji na mikataba ya walaji kwa wanafunzi wa Chuo Cha Ufundi Stadi VETA Kibaha ,ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Haki za Mlaji Duniani 2026.

Afisa Mlinda Mlaji Mwandamizi FCC Bi.Magdalena Hall,akitoa elimu kuhusu masuala ya kumlinda mlaji na mikataba ya walaji kwa wanafunzi wa Chuo Cha Ufundi Stadi VETA Kibaha ,ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Haki za Mlaji Duniani 2026.

Sehemu ya wanafunzi wa wanafunzi wa Chuo Cha Ufundi Stadi VETA Kibaha wakisikiliza mada mbalimbali wakati wakipata elimu kuhusiana na  masuala ya kumlinda mlaji na mikataba ya walaji kwa  ,ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Haki za Mlaji Duniani 2026.

Sehemu ya wanafunzi wa wanafunzi wa Chuo Cha Ufundi Stadi VETA Kibaha wakisikiliza mada mbalimbali wakati wakipata elimu kuhusiana na  masuala ya kumlinda mlaji na mikataba ya walaji kwa  ,ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Haki za Mlaji Duniani 2026.

Sehemu ya wanafunzi wa wanafunzi wa Chuo Cha Ufundi Stadi VETA Kibaha wakisikiliza mada mbalimbali wakati wakipata elimu kuhusiana na  masuala ya kumlinda mlaji na mikataba ya walaji kwa  ,ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Haki za Mlaji Duniani 2026.

Wanafunzi wa Chuo Cha Ufundi Stadi VETA Kibaha wakiuliza maswali mbalimbali kuhusu namna ya kutofautisha mikataba halisi na feki  mara baada ya kupatiwa elimu na FCC  ikiwa ni sehemu ya kuelekea Maadhimisho ya Wiki ya Siku ya Haki za Mlaji Duniani. 

Afisa Mlinda Mlaji Mwandamizi FCC Bi.Magdalena Hall,akiwa katika picha ya pamoja na wanafunzi wa Chuo Cha Ufundi Stadi VETA Kibaha mara baada ya kuwapatia elimu kuhusu masuala ya kumlinda mlaji na mikataba ya walaji kwa ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Haki za Mlaji Duniani 2026.

 



Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Songea (SOUWASA) imeendelea kudhihirisha ubora wake katika utoaji wa huduma baada ya kushika nafasi ya pili kwa miaka miwili mfululizo,  miongoni mwa mamlaka 20 za maji nchini zenye wateja zaidi ya 20,000, tuzo hizo  hutolewa na Mamlaka ya udhibiti wa huduma za nishati na maji(EWURA).

Mafanikio hayo yametokana na tathmini ya utendaji kwa mwaka wa fedha 2024/2025 inayofanywa na EWURA, ambayo hupima mamlaka za maji kwa kuzingatia vigezo mbalimbali ikiwemo ubora wa huduma kwa wateja, ukusanyaji wa mapato, upatikanaji wa maji safi na salama, pamoja na usimamizi wa miundombinu ya maji na majitaka.

Ripoti hiyo imezinduliwa rasmi na Waziri wa Maji, Jumaa H. Aweso, Machi 19, 2026, Mjini Morogoro, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali kuimarisha uwajibikaji na ufanisi katika sekta ya maji.

Ufanisi huu unatokana na mshikamano wa Bodi ya Wakurugenzi, watumishi wa mamlaka, pamoja na ushirikiano wa wananchi, sambamba na uwekezaji unaoendelea katika kuboresha huduma za maji katika Manispaa ya Songea.

Mafanikio haya yanaonyesha kuwa juhudi za pamoja na usimamizi thabiti vina mchango mkubwa katika kuinua kiwango cha huduma za maji, na yanaweka msingi imara wa kuendelea kuboresha zaidi huduma kwa wananchi.


 

Mamlaka za maji na usafi wa mazingira za Moshi, Nzega na Biharamulo zimetwaa tuzo za mamlaka bora nchini, katika tathmini ya ripoti ya EWURA ya utendaji wa mamlaka za maji iliyozinduliwa na Waziri wa Maji, Mhe. Jumaa Hamidu Aweso (Mb) leo tarehe 19 Machi 2026, mjini Morogoro.

Aidha, mamlaka 27 zilitambuliwa kwa kuwasilisha kwa asilimia 100 tozo ya udhibiti.

Taarifa ya hiyo ya Tathmini imepima Utendaji wa Mamlaka za Majisafi na Usafi wa Mazingira 83 zinazotoa huduma katika mikoa, wilaya na miji midogo , katika hafla iliyofanyika mjini Morogoro.

Waziri Aweso ameipongeza EWURA kwa kuandaa taarifa hiyo muhimu iliyobainisha uwazi, uwajibikaji na ufanisi katika utoaji huduma za maji na usafi wa mazingira nchini.

Kwa mujibu wa EWURA, tathmini hiyo imeonesha mafanikio katika ongezeko la uzalishaji wa maji kwa 19.3%, wateja kufikia milioni 1.8 na mapato kuongezeka kwa 14%. Hata hivyo, changamoto kama upotevu wa maji (42.3%) na uhaba wa miundombinu ya majitaka bado zinaendelea.

Mhe. Aweso amezitaka mamlaka za maji kuendelea kuboresha huduma kwa kuzingatia ubora, uwazi na uendelevu.

Kaimu Meneja wa Mkoa wa TRA Dodoma, Bw. Obrey Sillayo, akiambatana na Kaimu Meneja wa Huduma kwa Mlipakodi pamoja na maafisa wengine wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), wametoa mkono wa Eid Fitri kwa watoto yatima na wenye mahitaji maalumu katika Kituo cha Kulelea Watoto Yatima Rahmani, ikiwa ni sehemu ya kuonesha upendo na kuimarisha mshikamano na jamii.

Akizungumza wakati wa tukio hilo, Bw. Sillayo amepongeza juhudi za kituo hicho kwa kulea watoto katika misingi bora ya maadili na malezi, akisisitiza umuhimu wa kuendelea kuwajali watoto hao kwa ustawi wa taifa.

Aidha, ameeleza kuwa TRA itaendelea kushiriki katika shughuli za kijamii kama sehemu ya kuwajibika kwa jamii na kujenga uhusiano mzuri na wananchi.

Kwa upande wake, Bi. Rukia Hamisi Abdallah ameishukuru TRA kwa mkono huo wa Eid, akieleza kuwa umeleta faraja na matumaini kwa watoto wanaolelewa katika kituo hicho.

Tukio hilo limeacha ujumbe wa upendo, mshikamano na uwajibikaji kwa jamii.








Top News