Na Benny Mwaipaja, Horohoro, Tanga

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), ametoa wito kwa wafanyabiashara, wawekezaji na wazalishaji nchini kuongeza uzalishaji wenye tija na kuimarisha mauzo ya bidhaa katika masoko ya kimataifa ili kupunguza nakisi ya biashara (trade deficit) na kuongeza mchango wa sekta ya biashara katika kukuza uchumi wa Taifa.

Akizungumza wakati alipotembelea Kituo cha Huduma ya Pamoja Mpakani cha Horohoro, mkoani Tanga, ikiwa ni sehemu ya ziara yake mkoani humo, Mhe. Balozi Khamis alisema pamoja na mafanikio makubwa yaliyopatikana katika ukusanyaji wa mapato na uboreshaji wa mazingira ya biashara, bado ipo haja ya kuongeza thamani ya bidhaa zinazouzwa nje ya nchi ili Tanzania iweze kunufaika zaidi na biashara ya kimataifa.

Mhe. Balozi Omar alieleza kuwa takwimu za biashara kupitia Kituo cha Forodha cha Horohoro zinaonesha kuwa katika mwaka wa fedha uliopita bidhaa zenye thamani ya takribani shilingi bilioni 748 zilipitia katika kituo hicho, lakini kati ya hizo, bidhaa zilizouzwa nje ya nchi zilikuwa na thamani ya takribani shilingi bilioni 238 pekee, wakati bidhaa zilizoingizwa nchini zilifikia thamani ya shilingi bilioni 510, hali inayoonesha kuwepo kwa nakisi kubwa ya biashara.

"Matarajio ya kila taifa ni kuuza bidhaa nyingi zaidi kuliko linazoagiza kutoka nje, Takwimu hizi zinatuonesha bado tuna kazi kubwa ya kufanya katika kuongeza uzalishaji na kuimarisha mauzo ya bidhaa zetu nje ya nchi na Tanga ina fursa nyingi za uzalishaji na usafirishaji wa bidhaa, hivyo ni muhimu kuzitumia kikamilifu ili kupunguza nakisi hii," alisema Mhe. Balozi Khamis.

Alisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya biashara kupitia uwekezaji katika miundombinu ya forodha, mifumo ya kisasa ya ukaguzi wa mizigo pamoja na kuimarisha vituo vya mipakani ili kurahisisha biashara na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Aidha, alisema mafanikio ya ukuaji wa uchumi yanatoa msingi mzuri wa kuongezeka kwa shughuli za biashara nchini, akibainisha kuwa uchumi wa Tanzania ulikua kwa asilimia 5.9 mwaka 2025 na unatarajiwa kukua kwa asilimia 6.3 mwaka 2026, jambo litakalochochea ongezeko la uzalishaji na biashara.

Kwa upande wa ukusanyaji wa mapato, Mhe. Balozi Khamis alisema Kituo cha Huduma ya Pamoja Mpakani cha Horohoro, kimewekewa lengo la kukusanya shilingi bilioni 136 katika mwaka wa fedha 2026/27, baada ya kuvuka matarajio ya mwaka uliopita kwa kukusanya shilingi bilioni 125, hivyo kutokana na mwenendo mzuri wa ukuaji wa uchumi na biashara, Serikali ina imani kuwa lengo hilo litafikiwa, huku akibainisha kuwa kituo hicho kinachangia karibu robo ya mapato yote yaliyopangwa kukusanywa katika Mkoa wa Tanga.

“Serikali imetenga shilingi bilioni 573 katika Bajeti ya mwaka 2026/27 kwa ajili ya kuendeleza maboresho ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), ikiwemo ununuzi wa scanners (midaki) 27 za kisasa zitakazowekwa katika vituo mbalimbali vya forodha nchini, ikiwemo Kituo cha Forodha cha Horohoro” alisema Mhe. Balozi Omar

Alieleza kuwa mchakato wa ununuzi wa vifaa hivyo tayari umeanza na unafanyika kwa kuzingatia taratibu zote za ununuzi wa umma, huku akieleza kuwa vifaa hivyo hutengenezwa kwa kuzingatia mahitaji maalumu ya kila kituo cha forodha, hivyo mchakato wake unahusisha usanifu, utengenezaji, ukaguzi wa ubora, usafirishaji na ufungaji kabla ya kuanza kutumika na uwekezaji huo utaongeza ufanisi wa ukaguzi wa mizigo, kuharakisha utoaji wa huduma, kuimarisha usalama wa mipaka na kuongeza usahihi katika ukusanyaji wa mapato ya Serikali.

"Hatununui tu vifaa vya kisasa, bali tunawekeza katika kuongeza ufanisi wa biashara, kuimarisha usalama wa nchi na kuhakikisha Serikali inapata mapato yake stahiki, ma Midaki hii itasaidia kujua kwa uhakika bidhaa zinazopita mipakani, kupunguza muda wa ukaguzi na kurahisisha biashara halali," aliongeza Mhe. Balozi Omar.

Aliwahimiza pia wafanyabiashara kuendelea kutumia Kituo cha Huduma ya Pamoja Mpakani cha Horohoro, kufanya biashara halali na kuongeza mauzo ya bidhaa za Tanzania katika masoko ya nje, akisisitiza kuwa hatua hiyo itaongeza mapato ya fedha za kigeni, kupunguza nakisi ya biashara (trade deficit) na kuimarisha uchumi wa nchi.

Naye Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Tanga ambaye pia ni  Mkuu wa Wilaya ya Tanga mjini, Mhe. Dadi Kolimba, alisema Mkoa wa Tanga unaendelea kuwa miongoni mwa mikoa inayoongoza nchini katika ukusanyaji wa mapato, ukiwa wa sita kitaifa, mafanikio ambayo yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na utendaji mzuri wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) pamoja na ushirikiano wa taasisi nyingine za Serikali zinazofanya kazi katika vituo vya mipakani.

Alisema Kituo cha Forodha cha Horohoro ni miongoni mwa vituo muhimu vya kiuchumi vinavyochangia kwa kiwango kikubwa mapato ya Mkoa wa Tanga na Taifa kwa ujumla, akibainisha kuwa katika mwaka wa fedha uliopita kituo hicho kilivuka lengo lake kwa kukusanya shilingi bilioni 125 dhidi ya lengo la shilingi bilioni 115. Aliongeza kuwa Serikali ya Mkoa itaendelea kushirikiana na TRA kutatua changamoto zinazojitokeza, kuimarisha mazingira ya biashara na kuhamasisha uzalishaji pamoja na mauzo ya bidhaa za Tanzania katika masoko ya nje ili kuongeza mapato ya Serikali na kuchochea ukuaji wa uchumi.

Kwa Upande wao Naibu Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bw. Mcha Hassan Mcha, na Afisa Mfawidhi wa Kituo cha Huduma ya Pamoja Mpakani cha Horohoro, Bw. Shadrack Mbonea, walisema kuwa wamejipanga vyema kupambana na Magendo kwa kuimarisha doria za kimkakati kwa kushirikiana na taasisi nyingine za Serikali.

Walibainisha kuwa wataendelea kuimarisha ukaguzi wa mizigo inayoingia na kutoka nchini ili kuhakikisha wanatokomeza magendo lakini pia kuihakikisha kodi stahiki inakusanywa.

Katika Ziara hiyo Mhe. Balozi Omar aliambatana pia na, Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha ambaye pia ni Mhasibu Mkuu wa Serikali, CPA Leonard Mkude, Makamishna na maafisa waandamizi kutoka Wizara ya Fedha pamoja na taasisi zake.










Mbunge wa Jimbo la Dodoma Mjini Mhe. Paschal Inyasi Chinyele, amesema Serikali inaendelea kutekeleza hatua mbalimbali za kuboresha huduma za kijamii katika Kata ya Zuzu, akibainisha kuwa eneo hilo ni miongoni mwa maeneo yanayokua kwa kasi hivyo linahitaji uwekezaji zaidi katika miundombinu ya msingi, hususan huduma ya maji.

Akizungumza katika mkutano wa hadhara wa kutoa changamoto na kero mbalimbali zinazowakabili wananchi kwa mkuu wa mkoa wa Dodoma Julai 13, 2026, uliofanyika eneo la Chididimo lililopo Kata ya Zuzu Halimashauri ya Jiji la Dodoma, amesema kupitia Mfuko wa Jimbo la Dodoma Mjini, licha ya kugawana fedha na Jimbo la Mtumba katika mwaka wa fedha uliopita.

Amesema waliweza kutenga shilingi milioni 20 kwa ajili ya kuchimba kisima cha maji katika Shule za Msingi Chang’ombe na Milioni 20 zingine walichimba kisima katika shule ya msingi Chididimo, huku fedha za ujenzi wa kibanda cha kisima zikiwa zimepatikana kupitia nguvu ya wananchi na Halmashauri ya Jiji la Dodoma inatarajia kukamilisha miundombinu iliyobaki.

Mbunge huyo amesema upatikanaji wa maji ni kipaumbele kwa kuwa hakuna maisha bila maji, akisisitiza kuwa mradi huo utawanufaisha wananchi kwa kiasi kikubwa, aidha amesema Serikali imetoa shilingi milioni sita kwa ajili ya ujenzi wa maabara katika Hospitali ya Nzinje na shilingi milioni 46 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa shule ya sekondari, hatua itakayopunguza adha ya wanafunzi kutembea umbali mrefu na kukabiliwa na vihatarishi vinavyoweza kuathiri masomo yao ikiwemo utoro na mimba.

Awali, Diwani wa kata hiyo aliwasilisha changamoto zinazoikabili Zuzu na kuomba kukamilishwa kwa kipande cha barabara ya lami chenye urefu wa kilomita tano kinachoelekea Ring Road, ujenzi wa vivuko pamoja na soko la kisasa litakalowarahisishia wananchi kupata huduma za biashara karibu na makazi yao badala ya kutumia gharama kubwa za usafiri kufuata huduma hizo maeneo ya mbali.

Akizungumza katika ziara hiyo, Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma, Alimwoni Chaula, amepongeza utaratibu wa Mkuu wa Mkoa wa kutembelea wananchi na kusikiliza changamoto zao moja kwa moja, akisema hatua hiyo imeongeza kasi ya upatikanaji wa ufumbuzi wa kero mbalimbali na wananchi kuwa karibu na serikali Yao.

Amesema katika mwaka wa fedha 2026/2027, Jiji la Dodoma limetenga shilingi milioni 50 kwa kila eneo kwa ajili ya kujenga masoko katika maeneo yasiyo na huduma hiyo, huku Kata ya Zuzu ikiwa miongoni mwa maeneo yatakayonufaika, amesisitiza kuwa utekelezaji wa miradi hiyo utachochea maendeleo ya kiuchumi na kuboresha maisha ya wananchi wa Dodoma Mjini.












Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga (Mb), amemkabidhi mfanyabiashara mwenye ulemavu, Bi.Esther Mashaka Msengi, mashine ya kusagia viungo ili kuongeza uzalishaji, kupunguza gharama za biashara na kuboresha kipato chake.

Akikabidhi mashine hiyo katika Viwanja vya Maonyesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), amesema aliguswa na changamoto za Esther aliyekuwa akitumia muda na fedha nyingi kusafirisha viungo kwenda kusagwa kabla ya kuvifungasha na kuviuza.

Amesema Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi zake kuhakikisha anaimarisha biashara yake, huku akiitaka BRELA kukamilisha usajili wa nembo ya bidhaa zake, TBS kumsaidia kupata ithibati ya ubora na SIDO kuendelea kumjengea uwezo.

Aidha, amelishukuru Shirika la Uhandisi na Usanifu Mitambo Tanzania TEMDO kwa kuwezesha upatikanaji wa mashine hiyo na kueleza kuwa hatua hiyo inaunga mkono maono ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwawezesha wajasiriamali kuongeza tija.

Kwa upande wake, Bi. Esther Msengi amesema mashine hiyo itapunguza gharama za uzalishaji na kumwezesha kupanua biashara yake.

Mwakilishi wa Shirika la Uhandisi na Usanifu Mitambo Tanzania (TEMDO), Mhandisi. Elisante Mjema, amesema mashine hiyo inaweza kusaga kilo 10 za viungo kwa saa moja na kuongeza uzalishaji hadi kufikia mauzo ya takribani shilingi milioni 1.5 kwa siku endapo kutakuwa na malighafi za kutosha.

NA MWANDISHI WETU

Mwenyekiti Taifa wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), Mary Chatanda, amemshauri aliyewahi kuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Prof. Anna Tibaijuka, kuwa balozi wa kuhimiza viongozi na wananchi kutii sheria za nchi ili kuepuka kuingia katika mikono ya vyombo vya sheria.

Chatanda ameyasema hayo Julai 14, 2026, kufuatia ujumbe alioandika Prof. Tibaijuka katika Mtandao X, kuhusiana na kesi inayomkabili Mwenyekiti Taifa wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Tundu Lissu.

Katika ujumbe wake, Prof. Tibaijuka amesema "Dkt. Samia Suluhu, Mhe. Rais naendelea kushauri kwa dhati Tundu Lissu aachiwe huru kwani kesi haikamiliki, hekima na busara iliyotufanya kuitangaza sera ya 4Rs ulipoingia madarakani ikuongoze tena katika jambo hili".

"Simulizi hizi za kutisha za vyombo vya habari vya kimataifa zinainua hisia kali hasa kwa vijana, hata wazee tumekumbushwa kadhia ya operation Sogeza na iliyounda Vijiji vya Ujamaa 1974-1976, taarifa hizi zinaathiri kikubwa taswira ya Taifa letu na maslahi yake, athari ni kubwa".

"Tutafute muafaka kupitia uwajibikaji na maridhiano, tuwe na hofu ya Mungu na kutambua miujiza yake mfano wa risasi 16 kushindwa kukomesha uhai ingawa maumivu ni makubwa, tutubu na kusali kuliombea Taifa letu kila mtu kwa imani yake," ameongeza Prof. Tibaijuka katika andiko lake hilo.

Kutokana na andiko hilo, Chatanda amesema nchi inaongozwa kwa mujibu wa sheria na ni vyema mahakama iachwe ifanye kazi yake ili haki itendeke.

"Tusiruhusu utamaduni wa jambo linapokuwa mahakama, basi tuanze kumshinikiza Rais aingilie kati na kulimaliza. Tuiache mahakama ifanye kazi yake, na pale itakapothibitika kuwa mtuhumiwa hana hatia, basi ataachiwa huru," amesema Chatanda.

Sambamba na hilo, amesema, Tanzania ni nchi huru yenye mamlaka kamili na inaendesha mambo yake kwa mujibu taratibu zilizopo, hivyo hata vyombo vya habari vya kimataifa vinapaswa kuheshimu taratibu zetu za uendeshaji wa nchi na mashauri ya kisheria.

"Tusiruhusu kila kinachoandikwa katika vyombo vya habari vya kimataifa kikayumbisha na kusababisha kuacha kusimamia sheria za nchi, ni lazima tuheshimiane linapokuja suala la utii wa sheria za nchi," amesema.

Sanjari na hilo, Chatanda amesema, mataifa yaliyoendelea ni watii wazuri wa sheria zao, hivyo na sisi Watanzania tuwe na utamaduni wa kuheshimu sheria na mamlaka zilizopo na kutambua kuwa kamwe maridhiano si mbadala wa uvunjifu wa sheria.

"Dhana ya maridhiano isitumike vibaya, Rais Dk. Samia Suluhu Hassan amekuwa kinara wa maridhiano na hata alivyoingia madarakani aliwarejesha viongozi wa upinzani waliokuwa nje ya nchi, akawakaribisha warudi nyumbani ili nao watoe mchango wao katika ujenzi wa taifa, lakini baadhi yao ndo wamekuwa vinara wa kutoa kauli za kebehi na dharau kwa viongozi na serikali, hivyo tunapohimiza maridhiano, tusisahau pia utii wa sheria," amesema.

Katika hatua nyingine, Chatanda ametoa wito kwa wananchi kuendelea kuheshimu sheria za nchi ili kuepuka mkono wa sheria kwani nchi yetu inaongozwa kwa kuzingatia utawala wa sheria. Pia, amesisitiza umuhimu wa wananchi kulinda amani kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.



Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule, amewataka wazazi na walezi kujinyima mahitaji mengine ili kuhakikisha watoto wao wanapata elimu, akisisitiza kuwa elimu ndiyo msingi wa mafanikio katika dunia ya sasa inayohitaji watu wenye ujuzi na maarifa.

Akizungumza katika mkutano wa hadhara wa kusikiliza kero za wananchi uliofanyika Julai 13, 2026 katika eneo la Chididimo, Kata ya Zuzu, Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Senyamule amewapongeza wananchi wa kata hiyo kwa kuendelea kuboresha sekta ya elimu.

Amesema Shule ya Sekondari Zuzu, ambayo awali ilikuwa ya mwisho kimkoa kwa ufaulu, sasa imepanda hadi nafasi ya tisa kimkoa, jambo alilolitaja kuwa ni mafanikio makubwa.

Amesema mafanikio hayo yametokana na ushirikiano wa walimu, wazazi, wanafunzi na wadau wengine wa elimu, huku akisisitiza kuwa walimu hawawezi kufanikisha ufaulu bila wazazi kutekeleza wajibu wao wa kuhakikisha watoto wanahudhuria masomo kila siku.

Senyamule amesema Mkoa wa Dodoma umeendelea kufanya vizuri kitaifa katika elimu ya msingi kwa kushika nafasi ya pili, huku ukilenga kufikia nafasi ya kwanza kupitia ushirikiano wa karibu kati ya serikali, walimu na jamii.

Aidha, amewataka wazazi kuendelea kuiunga mkono serikali ambayo imewekeza katika ujenzi wa madarasa na miundombinu ya elimu, kwa kuhakikisha watoto hawakosi shule, amesema elimu si jambo la kusubiri bali ni uwekezaji unaoleta matokeo ndani ya muda mfupi.

Ameeleza kuwa watoto wanaopata elimu leo ndiyo watakaokuwa nguzo ya maendeleo ya vijiji, mitaa na kata katika miaka ijayo, kupitia maarifa na ujuzi watakaoupata shuleni.

Senyamule amesema zamani mtu aliweza kuishi bila elimu na akaendelea na maisha, lakini kwa kizazi cha sasa na kijacho hali hiyo haitakuwa rahisi kutokana na ongezeko la mahitaji ya wataalamu katika sekta mbalimbali, amesisitiza kuwa ni wajibu wa kila mzazi kuhakikisha mtoto anapata elimu ili aweze kushindana na kukabiliana na mahitaji ya dunia ya kisasa.






Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imekuletea mashindano ya Wazo Bunifu yanayolenga kupata suluhisho za kibunifu zitakazochangia kuboresha mfumo wa kodi nchini. Hii ni fursa yako ya kuwasilisha wazo lenye tija na kushindania zawadi ya hadi Shilingi Milioni 50.

Mawazo yatakayowasilishwa yanapaswa kulenga eneo moja au zaidi kati ya yafuatayo ; kupanua wigo wa kodi, kurahisisha ukadiriaji na ulipaji wa kodi kwa biashara ndogo ndogo, kuimarisha huduma za kodi za kidijitali, kupunguza gharama za ukusanyaji wa mapato, kutumia teknolojia za kisasa kama AI, Big Data na Blockchain katika usimamizi wa kodi, pamoja na kuboresha utatuzi wa migogoro ya kodi ili kuwa wa haraka, wazi na wenye kuaminika zaidi.

Kutuma Wazo lako ingia tovuti ya TRA, Bonyeza kitufe cha innovation portal fuata hatua zinazofuata, Mwisho wa kutuma wazo lako bunifu ni julai 31, 2026.

MWISHO WA SHINDANO HILI NI MWEZI HUU WA 7 NI HATARII


Kote nchini Tanzania, baa zina nafasi muhimu katika maisha ya kila siku ya jamii. Ni maeneo ambako marafiki hukutana, majirani hujumuika, mashabiki wa soka hutazama mechi pamoja, na biashara ndogo hukua.

Kupitia kampeni yake ya Cheers to Bars, Kampuni ya Tanzania Breweries Public Limited Company (TBL) inazitambua na kuzisherehekea baa kwa mchango wao katika kuwaleta watu pamoja na kusaidia uchumi mpana. Mbali na kuwa sehemu ambayo wateja hufurahia vinywaji, baa pia hutoa ajira kwa wamiliki, wahudumu, mabaa, wauzaji wa chakula, wasambazaji, wasafishaji, walinzi na watoa huduma za usafiri.

Kampeni hii pia inaangazia jinsi baa zinavyokuwa na umuhimu mkubwa zaidi wakati wa matukio makubwa ya michezo. Kadri hamasa ya soka inavyoendelea kuongezeka, mashabiki wengi huchagua kutazama mechi kwenye baa kwa sababu uzoefu huo huwa wa kuvutia zaidi unaposhirikishwa na wengine.

Katika Baa ya Kitambaa Cheupe jijini Dar es Salaam, mashabiki walikusanyika kushuhudia mechi ya robo fainali kati ya Hispania na Ubelgiji. Mechi hiyo ilikuwa mfano halisi wa jinsi baa za kienyeji zinavyobadilisha matukio ya soka ya kimataifa kuwa uzoefu wa pamoja wa kijamii. Mashabiki walitazama mchezo pamoja, wakashangilia, wakashiriki hisia na kuunda kumbukumbu za pamoja.

TBL inasema kuwa Cheers to Bars si kampeni inayohusu soka pekee. Ni kampeni inayotambua watu na biashara zinazowezesha maeneo ambayo yanaufanya mchezo wa soka kuwa sehemu ya maisha ya jamii.

"Baa ni sehemu muhimu ya maisha ya kijamii na kiuchumi ya Watanzania. Zinasaidia kujenga maisha ya watu, zinatoa fursa kwa biashara ndogo ndogo na zinatoa nafasi kwa jamii kukutana na kuimarisha mahusiano. Kupitia Cheers to Bars, tunazisherehekea baa hizi pamoja na watu wanaoziendesha, huku tukiwahamasisha watumiaji kufurahia vinywaji kwa kuwajibika," alisema Neema Temba, Mkurugenzi wa Sheria na Masuala ya Ushirika wa TBL.

Wakati wa mechi kubwa, baa yenye shughuli nyingi inaweza kunufaisha biashara zaidi ya moja. Wauzaji wa chakula, wasambazaji, watoa huduma za usafiri na timu mbalimbali za huduma zote hunufaika kutokana na ongezeko la shughuli. Hii inaifanya baa kuwa sehemu muhimu ya mfumo wa sekta ya ukarimu na burudani.

Mashabiki walipokusanyika katika baa ya Kitambaa Cheupe, mechi kati ya Hispania na Ubelgiji ilionyesha jinsi soka linavyowaunganisha watu na jinsi baa za kienyeji zinavyochangia kuunda uzoefu huo wa pamoja.

TBL inaendelea kuwahamasisha watumiaji kusherehekea kwa kuwajibika, kuunga mkono baa za kienyeji na kufurahia matukio ya soka katika mazingira salama na yenye furaha.

Kampeni ya Cheers to Bars ni ukumbusho kwamba baadhi ya kumbukumbu bora zaidi za soka hazitengenezwi uwanjani pekee. Pia huundwa katika baa za mitaani, ambako jamii hukusanyika, biashara hustawi na watu hushirikiana kufurahia mchezo.


















Serikali imeahidi kuhakikisha washiriki wa mafunzo ya ujasiriamali yanayotolewa na Jukwaa Huru la Wahariri Tanzania (JUWATA) wanayafanyia kazi kwa vitendo kwa kuwawezesha katika mikopo inayotolewa na Halmashauri kupitia utengenezaji wa bidhaa mbalimbali zitakazochangia ukuaji wa uchumi.

Kauli hiyo imetolewa mkoani Morogoro na Katibu Tawala Msaidizi Sehemu ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Beatrice Njawa, wakati akifungua mafunzo hayo kwa wananchi.

Bi.Njawa ambaye katika semina hiyo alimwakilisha Mgeni Rasmi, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Adam Malima amesema Serikali inataka kuona mafunzo hayo yanazaa matokeo ya moja kwa moja kwa washiriki kuanzisha na kuendeleza viwanda vidogo, kusindika mazao ya kilimo na kutengeneza bidhaa zenye ubora wa kushindana sokoni.

Mafunzo hayo ya siku tatu yanayoratibiwa na Jukwaa huru la Wahariri Tanzania (JUWATA) na kutolewa na wakufunzi wa taasisi ya MAMO ENTREPRNEURSHIP yanalenga kuwajengea wananchi mbalimbali uwezo wa kubuni miradi ya ujasiriamali itakayowaongezea kipato na kuchangia ajira kwa vijana.

Mbali na hayo Njawa amelipongeza JUWATA kwa kuona mbali na kuunga mkono juhudi za Serikali za kujenga uchumi wa viwanda. “Habari peke yake haitoshi. Amesema kuwa Mwandishi wa habari anaweza kuwa mtengenezaji wa bidhaa na mtumishi wa umma anaweza kuwa mjasiriamali huo ndio mwelekeo wa taifa,” amesema Bi.Njawa.

Katika hatua nyingine Bi.Njawa ameeleza kuwa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro kupitia Sehemu ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji itafanya ufuatiliaji wa karibu kuhakikisha washiriki wanatekeleza waliyojifunza na kuahidi kuwa vikundi vitakavyofanya vizuri vitapewa kipaumbele na mwakani 2027 watapelekwa katika maonesho ya Sabasaba.

Mafunzo hayo ni sehemu ya mkakati wa JUWATA wa kuwajengea wanachama wake uwezo wa kujitegemea kiuchumi sambamba na kutekeleza majukumu yao ya kuhabarisha umma.

















Top News