Na Eva Ngowi, Harare, Zimbabwe

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), ameongoza ujumbe wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Mkutano wa Kamati ya Mawaziri wa Fedha na Uwekezaji wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), unaofanyika jijini Harare, Zimbabwe, ambapo Tanzania imewasilisha msimamo wake kuhusu utekelezaji wa Mfuko wa Maendeleo wa Kikanda wa SADC (SADC Regional Development Fund) pamoja na mapendekezo ya vyanzo mbadala vya kugharamia miradi na programu za maendeleo za kikanda.

Akizungumza baada ya kikao hicho kilichowakutanisha Mawaziri wa Fedha, Magavana wa Benki Kuu na viongozi waandamizi wa sekta za fedha kutoka nchi 16 wanachama wa SADC, Mhe. Luswetula alisema pamoja na kujadili ajenda mbalimbali za maendeleo ya uchumi wa kikanda, Tanzania ilijielekeza katika masuala mawili yenye umuhimu wa kipekee kwa maslahi ya taifa.

Alieleza kuwa suala la kwanza lilihusu utekelezaji wa Mfuko wa Maendeleo wa Kikanda wa SADC, ambapo Tanzania ilieleza kuwa iliridhia mkataba wa Mfuko huo mwaka 2016 na kwa sasa inaendelea kukamilisha taratibu za ndani zitakazoruhusu kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wake.

Aidha, Tanzania ilitoa msisitizo kuwa pamoja na kwamba Mfuko huo ni muhimu katika Ukanda wa SADC, hata hivyo bado kuna changamoto hususan ya upatikaji wa mtaji wa kuanzia kutoka kwa nchi wanachama kutokana na changamoto za kiuchumi walizonazo.

"Tumeeleza kuwa baada ya kukamilika kwa taratibu zote za ndani, Serikali itaijulisha rasmi Sekretarieti ya SADC ili Tanzania iweze kuanza kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa Mfuko wa Maendeleo wa Kikanda," alisema Mhe. Luswetula.

Alisema suala la pili lilihusu mapendekezo ya kutumia tozo za utalii (Tourism Levy) pamoja na ushuru wa forodha (Import levy) kama vyanzo vya kugharamia bajeti, miradi na programu za maendeleo za SADC, ambapo Tanzania ilieleza kuwa mapendekezo hayo yanahitaji kuangaliwa kwa kina zaidi.

Mhe. Luswetula alifafanua kuwa matumizi ya mapato yanayotokana na ushuru wa forodha kwa madhumuni hayo yanakinzana na mfumo wa usimamizi wa mapato nchini Tanzania, kwa kuwa Sheria ya Usimamizi wa Kodi ya mwaka 2015, iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2023, inaelekeza kuwa mapato yote yanayokusanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania yaingizwe katika Mfuko Mkuu wa Serikali.

Aidha, alisema Serikali ya Tanzania imeeleza kuwa matumizi ya tozo za utalii yanaweza kuongeza gharama za utalii nchini, jambo ambalo linaweza kupunguza ushindani wa sekta hiyo na kuathiri jitihada za kuvutia watalii wengi zaidi.

Kutokana na hali hiyo, Tanzania ilipendekeza nchi wanachama ziongeze uwajibikaji kwa kuwasilisha michango yao kwa wakati na kuhakikisha nchi ambazo bado hazijatekeleza wajibu huo wa kimkataba zinatimiza ahadi zao, badala ya kuanzisha tozo mpya zitakazoweza kuathiri uchumi wa nchi wanachama.

"Tunaamini njia endelevu ni kuhakikisha kila nchi inatimiza wajibu wake wa kuchangia bajeti ya SADC kwa wakati ili kuwezesha utekelezaji wa miradi na programu za maendeleo ya kikanda," alisema Mhe. Luswetula.

Mbali na masuala ya sera za fedha, Mhe. Luswetula alisema mkutano huo umeendelea kufungua fursa mpya za biashara na uwekezaji kwa nchi wanachama, huku akiwasihi wafanyabiashara wa Tanzania kutumia ipasavyo soko la SADC lenye nchi 16 na watu zaidi ya million 417 kwa kupanua biashara zao katika sekta mbalimbali, hususan kilimo, biashara na huduma.

Aidha, alibainisha kuwa Tanzania itaendelea kuimarisha sekta ya utalii kwa kutumia fursa zilizopo ndani ya ukanda huo, akieleza kuwa mafanikio yaliyopatikana kupitia kampeni ya Royal Tour iliyoanzishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, yameongeza idadi ya watalii wanaoitembelea Tanzania.

"Kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, tutaendelea kuongeza nguvu katika kuitangaza Tanzania ili iwe kitovu cha utalii barani Afrika," alisema Mhe.Luswetula.

Mkutano huo wa Kamati ya Mawaziri wa Fedha na Uwekezaji wa SADC umejadili masuala mbalimbali ya ushirikiano wa kifedha, uwekezaji, biashara na maendeleo ya kikanda, huku ukilenga kuimarisha ustahimilivu wa uchumi wa nchi wanachama na kuharakisha utekelezaji wa programu za maendeleo chini ya Ajenda ya Maendeleo ya Kikanda ya SADC.

Mkutano huo ulifunguliwa rasmi na Mwenyekiti wa Kamati ya Mawaziri wa Fedha na Uwekezaji wa SADC ambaye pia ni Waziri wa Fedha wa Jamhuri ya Afrika Kusini, Mhe. Enoch Godongwana; ambapo alizitaka nchi wanachama kuimarisha ushirikiano wa kikanda katika kukabiliana na changamoto za uchumi wa dunia, kuendeleza vyanzo endelevu vya ufadhili wa maendeleo, pamoja na kuharakisha utekelezaji wa miradi ya kimkakati itakayochochea ukuaji wa uchumi, biashara na uwekezaji ndani ya ukanda wa SADC.
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), ambaye anaongoza ujumbe wa Tanzania katika Mkutano wa Mawaziri wa Fedha na Uwekezaji wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), akisikiliza kwa makini wakati wa ufunguzi wa mkutano wa maazimio na mapendekezo yaliyofikiwa na vikao vya Makatibu Wakuu wa Hazina, wakati wa vikao vya SADC vinavyoendelea jijini Harare, Zimbabwe.

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), (wa sita kulia) katika picha ya pamoja na Mawaziri wa Fedha na Magavana wa Benki Kuu wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), wakati wa vikaovinavyoendelea jijini Harare, Zimbabwe.

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), (kulia), akifuatilia hotuba ya ufunguzi wa mkutano wa maazimio na mapendekezo wa Mawaziri wa Fedha, Uwekezaji na Afya. Kushoto ni Naibu Waziri Naibu Waziri, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Mhe. Dkt. Pius Chaya (Mb).

Ujumbe kutoka Tanzania ukifuatailia ufunguzi wa mkutano wa Mkutano wa Mawaziri wa Fedha na Uwekezaji wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC unaoendelea Harare nchini Zimbabwe.

Mkutano wa Kamati ya Mawaziri wa Fedha na Uwekezaji wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), unaofanyika mjini Harare, Zimbabwe, ukiwakutanisha Mawaziri wa Fedha, Magavana wa Benki Kuu na Maafisa Waandamizi wa Hazina kutoka nchi wanachama.


Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), (kulia) akifurahia jambo wakati wakibadilishana Mawazo na Balozi wa Tanzania nchini Zimbabwe Mhe, CP Suzan Kaganda, (kushoto) pamoja na Mkurugenzi wa Kanda ya Afrika wa Shirika la Afya Duniani – WHO, Prof. Mohamed Yakub Janabi wakati wa mapumziko ya Vikao vya Mikutano ya Kamati ya Mawaziri wa Fedha na Uwekezaji wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) inayoendelea Harare nchini Zimbabwe.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha)



Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba ameweka jiwe la msingi la Hospitali ya Wilaya ya Butiama Kizurira Nyerere wilayani Butiama, mkoani Mara, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Hospitali hiyo imejengwa kwa lengo la kuboresha upatikanaji wa huduma za afya kwa wananchi wa Wilaya ya Butiama na maeneo ya jirani, ambapo awali walilazimika kusafiri umbali mrefu kufuata huduma katika hospitali za wilaya nyingine.

Taarifa ya mradi iliyowasilishwa kwa Waziri Mkuu ilieleza kuwa hadi sasa Halmashauri ya Wilaya ya Butiama imepokea jumla ya shilingi bilioni 3.66 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali hiyo, fedha zilizotolewa na Serikali Kuu pamoja na mapato ya ndani ya halmashauri. Ujenzi unaendelea kwa mfumo wa Force Account, huku baadhi ya majengo yakikamilika na kuanza kutoa huduma na mengine yakiwa katika hatua mbalimbali za ukamilishaji.

Majengo yaliyokamilika ni pamoja na jengo la wagonjwa wa nje (OPD), maabara, jengo la dharura, jengo la upasuaji, wodi ya wazazi na kichomea taka za hospitali. Aidha, ujenzi wa jengo la utawala, wodi za wanaume na wanawake, jengo la mionzi, bohari ya dawa na kufulia unaendelea.

Akizungumza katika hafla hiyo, Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Dkt. Festo Dugange alisema Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika miundombinu ya afya nchini.

Alisema hadi mwaka 2020 kulikuwa na hospitali za halmashauri 55 pekee tangu Uhuru, lakini katika kipindi cha miaka sita ya Serikali ya Awamu ya Sita zimejengwa hospitali za halmashauri 129, hatua iliyowezesha halmashauri zote 184 nchini kuwa na hospitali zenye miundombinu bora na ya kisasa.

Aidha, alisema Serikali imetenga shilingi milioni 500 katika mwaka wa fedha 2026/2027 kwa ajili ya kukamilisha majengo yaliyosalia katika Hospitali ya Wilaya ya Butiama ili huduma zote muhimu zianze kutolewa kwa wananchi.

Hospitali hiyo inatarajiwa kuongeza uwezo wa utoaji wa huduma za wagonjwa wa nje, upasuaji, huduma za mama na mtoto, maabara, mionzi, tiba ya viungo pamoja na huduma nyingine muhimu za kibingwa, hivyo kupunguza rufaa zisizo za lazima kwenda hospitali za nje ya wilaya.














Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Serikali imeahidi kuendelea kuimarisha huduma za usafi wa mazingira nchini kwa kuhakikisha kila Mtanzania, mijini na vijijini, anapata huduma bora zitakazochangia kulinda afya za wananchi, kuhifadhi mazingira na kuchochea maendeleo endelevu.

Kauli hiyo imetolewa leo Jijini Dodoma wakati wa Kongamano la Kitaifa la Usafi wa Mazingira, lililoambatana na uzinduzi wa Mwongozo wa Mipango Jumuishi ya Usafi wa Mazingira wa mwaka 2025, unaolenga kuunganisha juhudi za serikali na wadau mbalimbali katika kuboresha usimamizi wa taka ngumu, majitaka na huduma nyingine za usafi wa mazingira nchini.

Akizungumza katika kongamano hilo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Profesa Paramagamba Kabudi, amesema usafi wa mazingira ni msingi muhimu wa afya ya jamii na maendeleo ya taifa, hivyo Serikali imeweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha huduma hizo zinawafikia wananchi wote bila ubaguzi.

Amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan imeendelea kutoa kipaumbele kikubwa katika uhifadhi wa mazingira na utekelezaji wa sera zinazolenga kujenga miji na vijiji vilivyo safi, salama na endelevu.

"Maendeleo ya taifa hayawezi kutenganishwa na mazingira safi. Tunahitaji kujenga utamaduni wa usafi kwa kushirikisha wananchi wote ili kuhakikisha Tanzania inakuwa na miji na vijiji vinavyovutia na vinavyolinda afya za wananchi," amesema Prof. Kabudi.

Aidha, amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kuboresha mifumo jumuishi ya usimamizi wa taka na majitaka ili kupunguza magonjwa yanayotokana na uchafuzi wa mazingira pamoja na kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma za usafi nchini.

Prof. Kabudi pia amempongeza Rais Samia kwa kuiongoza Tanzania katika ajenda ya matumizi ya nishati safi, akieleza kuwa hatua hiyo imeifanya nchi kuwa miongoni mwa mataifa yanayoongoza juhudi za matumizi ya nishati rafiki kwa mazingira.

Amesema matumizi ya nishati safi yanapaswa kuendelea kuhamasishwa ili wananchi wengi zaidi waweze kutumia teknolojia zinazolinda afya na mazingira.

Waziri huyo pia amekosoa tabia ya baadhi ya wananchi kutupa taka kwenye mitaro ya maji, akieleza kuwa hali hiyo husababisha kuziba kwa mifereji, kuongezeka kwa mafuriko pamoja na kuibuka kwa magonjwa yanayoweza kuzuilika.

Ameongeza kuwa uwekezaji katika sekta ya usafi wa mazingira ni uwekezaji wa moja kwa moja katika afya ya wananchi, huku akihimiza ulinzi wa vyanzo vya maji na utekelezaji madhubuti wa sheria na kanuni za mazingira.

Kwa upande wa huduma za kijamii, Prof. Kabudi amesisitiza umuhimu wa kuboresha miundombinu ya vyoo katika maeneo ya mikusanyiko kama masoko, vituo vya mabasi na maeneo mengine ya umma, pamoja na kuhakikisha upatikanaji wa maji na vifaa vya kunawa mikono ili kuzuia magonjwa ya mlipuko.

Akitaja changamoto zinazoikabili sekta hiyo, amesema ongezeko la makazi holela na athari za mabadiliko ya tabianchi vinahitaji mipango bora ya matumizi ya ardhi, upimaji wa viwanja na usimamizi madhubuti wa maendeleo ya makazi.

Naye Kaimu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira, Kunti Majala, amesema elimu ya mazingira inapaswa kupewa nafasi kubwa zaidi kwa kuwa sehemu kubwa ya madhara yanayosababisha vifo hutokana na shughuli za binadamu ambazo zinaweza kudhibitiwa kupitia uelewa sahihi wa jamii.

Majala ameipongeza EWURA kwa kuandaa kongamano hilo, akisema limefungua ukurasa mpya wa maboresho katika usimamizi wa huduma za usafi wa mazingira nchini.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Fedha wa EWURA, Stanley Mahembe, amesema bado kuna changamoto kubwa katika usimamizi wa majitaka, ambapo takwimu zinaonyesha kuwa kati ya mamlaka 84 za maji nchini, ni mamlaka 24 pekee zenye mipango ya kutibu majitaka na tope la kinyesi.

Amesema uzinduzi wa mwongozo mpya utasaidia kuongeza ufanisi wa usimamizi wa huduma hizo na kuimarisha ufuatiliaji wa utekelezaji wake katika mamlaka mbalimbali.

"EWURA itaendelea kushirikiana kwa karibu na Serikali pamoja na wadau wengine kuhakikisha huduma za usafi wa mazingira zinaendelea kuboreshwa kwa manufaa ya afya za wananchi na uhifadhi wa mazingira," amesema Mahembe.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Jabir Shekimweri, amesema ongezeko la kasi ya ukuaji wa idadi ya watu katika mkoa huo limeongeza mahitaji ya huduma bora za usafi wa mazingira, huku akiahidi kuwa wilaya hiyo ipo tayari kutekeleza miongozo mipya ili kuhakikisha mazingira yanabaki salama na yenye afya kwa wananchi.








NAIBU Waziri wa Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe Rueben Kwagilwa akizungumza na vyombo vya habari Julai 2,2026 Jijini Tanga kuhusu tamko la Serikali kuhusiana na maandalizi ya Mkutano wa 12 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Nairobi (COP 12) unaotarajiwa kufanyika Kuanzia Octoba 6 hadi 9 Mwaka huu
Serikali imezitaka Wizara, Taasisi za Umma, Sekta Binafsi, Watafiti na Mashirika ya Kiraia kuchangamkia fursa ya Tanzania kuwa mwenyeji wa 12 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Nairobi (COP 12).

Hayo yamesemwa leo Julai 2, 2026 Jijini Tanga na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Reuben Kwagilwa wakati akitoa tamko la Serikali kuhusu maandalizi ya Tanzania kuelekea Mkutano huo unaotarajia kufanyika nchini kuanzia tarehe 6-9 Oktoba mwaka huu.

Mkuu wa Mkoa wa Tanga Balozi,Dkt Batilda Burian akionesha kitabu chenye taarifa ya utafiti kuhusu masuala ya mazingira mkoani humo wakati wa mkutano wa Naibu Waziri Ofisi ya Makau a Rais (Muungano na Mazingira )Mhe Rueben Kwagilwa na waandishi wa habarai Julai 2 mwaka huu kuhusu tamko la Serikali kuhusu maandalizi ya mkutano wa 12 wa nchi wanachama wa mkataba awa Nairobi (COP 12) unaotarajiwa kufanyika nchini kuanzia Octoba 6-9 mwaka huu


Naibu Waziri Kwagilwa amesema katika Mkutano wa 11 wa Nchi Wanachama uliofanyika nchini Madagasca mwaka 2024, Tanzania ilichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Kamati Tendaji ya Mkataba wa Nairobi kwa kipindi cha miaka miwili hadi Disemba Mwaka 2026 pamoja na kuteuliwa kuwa mwenyeji wa COP12.


“Mkutano wa COP12 utajadili utekelezaji wa Mpango Kazi wa Mkataba kwa kipindi cha mwaka 2024–2026 pamoja na kujadili masuala muhimu ikiwemo hifadhi na urejeshwaji wa mifumo ikolojia ya bahari kama mikoko, miamba ya matumbawe na nyasi bahari” amesema Mhe. Kwagilwa.

Baadhi ya watendaji waandamizi kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais wakifuatilia tamko la Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira ) Mhe.Rueben Kwagilwa wakati alipozungumza na waandishi wa habari Jijini Tanga kuhusu maandalizi ya mkutano wa 12 wa nchi wanachama wa mkataba awa Nairobi (COP 12) unaotarajiwa kufanyika nchini kuanzia Octoba 6-9 mwaka huu

Ameongeza kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeendelea kuipa kipaumbele sekta ya mazingira na uhifadhi wa rasilimali za bahari ili kuimarisha uhifadhi wa rasilimali za bahari, mito, maziwa, maji chini ya ardhi na maeneo oevu.

Wadau wa Mazingira na Wananchi wa Mkoa wa Tanga wakifuatilia tamko la Naibu Waziri wa Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe Reuben Kwagilwa wakati alipozungumza na waandishi wa habari Jijini Tanga kuhusu maandalizi ya mkutano wa 12 wa nchi wanachama wa mkataba awa Nairobi (COP 12) unaotarajiwa kufanyika nchini kuanzia Octoba 6-9 mwaka huu

Kwa mujibu wa Naibu Waziri Kwagilwa, amesema Dira 2050 imeitambua sekta ya uchumi wa Buluu kuwa miongoni mwa sekta za kimkakati zinazokusudia kuleta mageuzi ya maendeleo endelevu na kuchangia ukuaji wa kijamii, kiuchumi na kiikolojia.


Amesema kuwa Tanzania ni nchi ya pwani yenye fursa kubwa ya kunufaika na sekta ya uchumi wa buluu kupitia uvuvi, nishati, usafirishaji, utalii, madini, mazingira na viwanda, hivyo mkutano huo utaliwezesha taifa kuwa katika nafasi bora ya kufikia maendeleo endelevu.


Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Balozi Dkt. Batilda Burian amesema matokeo ya utafiti uliofanyika mkoani humo yanaonyesha athari za mabadiliko ya tabianchi zimeanza kuathiri kwa kiwango kikubwa shughuli za uvuvi na ukuzaji wa viumbe maji, hususan kilimo cha mwani.

Amesema utafiti uliofanyika kati ya mwaka 2021 na 2025 umebaini kuwa joto la bahari limeongezeka kutoka nyuzi joto 25.6 mwaka 2021 hadi kufikia nyuzi joto 28.39 mwaka 2024, hali inayobadili mfumo wa ikolojia wa bahari na kuathiri uzalishaji katika sekta ya uvuvi.


"Tumeshuhudia ongezeko la karibu nyuzi joto tatu baharini, huku siku za wavuvi kwenda kuvua zikishuka kutoka siku 221 mwaka 2021 hadi siku 170 kutokana na upepo mkali na hatari ya usalama baharini. Pia mavuno ya samaki yamepungua kwa wastani wa asilimia 25 hadi 30," amesema Dkt. Burian.

Awali akimkaribisha mgeni rasmi, Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Ofisi ya Makamu wa Rais, Balozi Baraka Luvanda amesema mkutano wa COP 12 utahusisha washiriki takribani 500-600 ikiwemo viongozi wa nchi, wataalamu na wadau mbalimbali.

Ameongeza kuwa lengo la tamko hilo la Serikali ni kuweka msingi wa maandalizi ya kina, ikiwa ni pamoja na kubainisha vipaumbele vya Taifa, na kupanga mikakati ya ushiriki ili kuhakikisha maandalizi yanafanyika kwa ufanisi na kwa wakati.

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni nchi mwanachama wa Mkataba wa Nairobi unaohusu Hifadhi, Usimamizi na Uendelezaji wa Mazingira ya Bahari na Ukanda wa Pwani wa Magharibi mwa Bahari ya Hindi.

Mkataba huu ulisainiwa tarehe 21 Juni 1985 na unatekelezwa chini ya usimamizi wa Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEP).




Mkurugenzi wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB), Bw. Asangye Bangu, amewataka waendesha maghala kuzingatia uadilifu, uwajibikaji na utoaji wa huduma bora ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala.

Akifungua kikao maalumu cha waendesha maghala kilichofanyika mjini Morogoro Julai 1, 2026, Bangu, amesema waendesha ghala wanapaswa kuendana na wakati kwa kuwa waadilifu, kutoa huduma zenye viwango vya juu na kuhakikisha mfumo wa stakabadhi za ghala unaendelea kuwa na tija kwa wakulima, wafanyabiashara na wananchi kwa ujumla.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Waendesha ghala Tanzania, Abdulikarim amesema kikao hicho kimeandaliwa kwa lengo la kuongeza uelewa kuhusu masuala mbalimbali ya kiutendaji, kujadili changamoto zinazowakabili pamoja na kutafuta suluhisho la kuboresha maslahi ya waendesha ghala kutokana na kupanda kwa gharama za maisha na uendeshaji wa shughuli zao.

Ameongeza kuwa maazimio na maelekezo yaliyotolewa katika kikao hicho yatawasaidia waendesha ghala kuongeza ufanisi wa kazi zao na kuendelea kutoa huduma bora kwa wadau wote wa sekta ya kilimo.

Top News