📍 Ni zile familia 67 zilizobomolewa nyumba na Amboni Plantation
Na Mwandishi Wetu, Kigombe
MBUNGE wa Muheza, Mhe. Hamis Mwinjuma (MwanaFA), amewahakikishia wananchi wa kaya 67 waliobomolewa nyumba zao na Kampuni ya Amboni Plantation kuwa watalipwa fidia zao kikamilifu.
Uharibifu huo wa dharura ulioacha familia hizo za Kitongoji cha Maisha Plus mkoani Tanga zikilala nje, ulifanyika mwishoni mwa wiki iliyopita kwa madai ya wananchi hao kuvamia eneo la shamba la mkonge la mwekezaji huyo.
Akizungumza jana Mei 29, 2026 aliporejea kijijini hapo kutoa mrejesho wa kikao chake cha ndani na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dkt. Batilda Burian, MwanaFA alisema Serikali imejipanga vizuri kulinda utu wa wanyonge hao.
"Sitaki kuwaambia ni kiasi gani mtalipwa, lakini sisi kama viongozi wenu tunawahakikishia jambo lenu litakwenda vizuri na mtalipwa fidia kabla ya kuondoka hapa. Suala hili linanikosesha usingizi na sitarudi kwenye majukumu ya kitaifa hadi dharura hii iishe," alisema MwanaFA.
Mbunge huyo, ambaye pia ni Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, alisema ameshazungumza na taasisi zinazosimamia majanga nchini ili kuleta mahema ya kisasa yatakayotumika kama makazi ya muda ya dharura kujikinga na mvua za mchoo.
Kuhusu mchakato wa kisheria, Mhe. Mwinjuma alibainisha kuwa Mkuu wa Mkoa anaunda Tume Maalum kupitia upya hukumu ya kesi hiyo na namna ubomoaji ulivyotekelezwa.
Maazimio mengine ya dharura yaliyofikiwa ni pamoja na kuwataka waliohusika na ubomoaji huo kuwajibishwa kwa kufanya oparesheni bila taarifa kwa Serikali, kumlazimisha mwekezaji asafishe eneo jipya, kuwapa wananchi hati, na kutoa fedha za "kifuta machozi".
Hata hivyo, wananchi wa eneo hilo wametoa kasoro mpango wa kuhamishiwa kwenye ardhi mpya yenye ekari 37 iliyotolewa na mwekezaji, wakidai haina sifa za makazi ya binadamu.
Mwananchi Ernest John, alitahadharisha kuwa eneo hilo ni mkondo wa asili wa njia za maji, huku Hamad Hamza akibainisha kuwa limefichama porini na halina huduma za msingi.
"Huko tunakopelekwa ni porini, hakuna shule wala zahanati. Tunaomba Serikali ituchagulie maeneo ya kwenda kukaa, lakini yawe karibu na vijiji vya Pangani kule Kimang'a au Kwasawaka ili watoto wetu wapate huduma, na sio kututupa kwenye hatari ya mafuriko kwa maelekezo ya mwekezaji," alilalamika mkazi Jane Sekela Msigalo.
Mhe. Mwinjuma alituliza mzuka na kuahidi kuwa wataalamu wa ardhi na mazingira watafanya vipimo vya kitalamu vya udongo kwanza, na kama eneo hilo lina changamoto ya maji halitotumika.
Katika mkutano huo, Diwani wa Kata ya Kigombe, Mhe. Shahongwe Mgandi, alimshukuru Mkuu wa Mkoa kwa kupeleka kitoweo cha ng'ombe wa sikukuu ya Eid El-Adha kwa wahanga hao, akisihi suluhu ya kudumu ipatikane haraka.
Malalamiko makubwa yaliibuka dhidi ya mgambo waliotekeleza oparesheni hiyo, ambapo mwananchi Jane Francis Raphael, alijeruhiwa vibaya baada ya kusukumwa kwa nguvu na mgambo mmoja wakati akijaribu kuokoa mali zake zisiibwe.
Mbunge MwanaFA alihitimisha kwa kuwapoza wananchi na kuahidi kuwa atakuwa nao bega kwa bega hadi haki yao ya kikatiba na kisheria itakapopatikana nchini.