Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, ameieleza Jumuiya ya Kimataifa hatua kubwa zinazochukuliwa na Serikali ya Tanzania katika kulinda na kuendeleza haki za watu wenye ulemavu, wakati aliposhiriki Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19) unaofanyika katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, Jijini New York, Marekani.

Mhe. Mahundi, ambaye amemuwakilisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu–Sera, Bunge na Uratibu  na Wenye Ulemavu, Mhe. Profesa Palamagamba John Kabudi, amesema Tanzania imeendelea kuimarisha mifumo ya kisheria, kisera na kiutendaji ili kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata haki, fursa na huduma stahiki kama wananchi wengine.

Akiwasilisha taarifa ya nchi, Mhe. Mahundi amesema Tanzania imepiga hatua kubwa kupitia Sheria ya Watu Wenye Ulemavu Na. 9 ya mwaka 2010 kwa Tanzania Bara pamoja na Sheria Na.8 ya mwaka 2022 ya Zanzibar, ambazo zimeweka msingi imara wa kulinda haki na ustawi wa watu wenye ulemavu.

 “Masuala ya ulemavu yamejumuishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na mipango mbalimbali ya maendeleo ili kuhakikisha hakuna anayebaki nyuma katika safari ya maendeleo ya taifa na kusema kuwa Serikali imeendelea kupanua upatikanaji wa elimu jumuishi, huduma za afya, huduma za urekebishaji na tiba, teknolojia saidizi, programu za uwezeshaji kiuchumi pamoja na huduma za hifadhi ya jamii kwa watu wenye ulemavu” @maryprisca_mahundi.

Aidha  Mhe. Mahundi amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa uongozi wake madhubuti na dhamira ya dhati ya kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata huduma bora na fursa zinazowawezesha kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya nchi.

Mkutano huo wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu umebeba kaulimbiu inayosema “CRPD at 20: Celebrating and Consolidating Achievements and Shaping the Next Phase of Implementation in a Changing World,” ukilenga kutathmini mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 20 tangu kuanzishwa kwa mkataba huo na kuweka mikakati.







Bohari ya Dawa (MSD) imeihakikishia Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI kuwa itaendelea kuimarisha upatikanaji wa bidhaa za afya zenye ubora, kwa wakati na kwa kiwango kinachohitajika kuelekea utekelezaji wa awamu ya pili ya Bima ya Afya kwa Wote.

Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi Mkuu wa MSD, Mavere Tukai, mbele ya Kamati hiyo Juni 9, 2026 mara baada ya wajumbe wa Kamati hiyo kufanya ziara katika Ghala Kuu la MSD Dodoma kwa lengo la kujionea shughuli za kila siku za taasisi hiyo katika uzalishaji, ununuzi, uhifadhi na usambazaji wa bidhaa za afya.

“Sisi tumeshajipanga, na utayari wetu unategemea kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa rasilimali. Tayari tumewasilisha mahitaji yetu Serikalini kwa ajili ya kuwezesha utekelezaji wa mpango wa Bima ya Afya kwa Wote na kuhakikisha wananchi wanapata huduma zinazostahili,” amesema Mavere.

Amesema MSD inaendelea kujiandaa kukidhi ongezeko la mahitaji ya bidhaa za afya litakalotokana na utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote, huku akibainisha kuwa bidhaa za afya zenye thamani ya zaidi ya Shilingi trilioni 1.2 hununuliwa kupitia MSD na kusambazwa katika vituo vya kutolea huduma za afya nchini.

Katika ziara hiyo, wajumbe wa Kamati walipata maelezo kuhusu mifumo ya ugavi wa bidhaa za afya, hatua zinazochukuliwa kuhakikisha upatikanaji wa bidhaa hizo nchini pamoja na mifumo ya udhibiti wa ubora inayotekelezwa kwa kushirikiana na mamlaka mbalimbali ikiwemo Mamlaka ya Dawa na VifaaTiba (TMDA) na taasisi nyingine za ndani na nje ya nchi.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI, Mhe. Johannes Lukumay, ameipongeza MSD kwa kazi kubwa inayofanya ya kuhakikisha wananchi wanapata bidhaa za afya zenye ubora na kwa wakati, huku akiitaka taasisi hiyo kuendelea kuimarisha mifumo yake ili kukidhi mahitaji yanayoongezeka ya huduma za afya nchini.

Naye Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Dkt. Zeyana Abdallah Hamid, ameutaka uongozi wa MSD kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu shughuli za taasisi hiyo ili wananchi waweze kufahamu thamani ya uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali katika kuhakikisha bidhaa za afya zinapatikana kwa uhakika nchini.








 

Na Mwandishi Wetu

Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB), Asangye Bangu, ameshiriki Jukwaa la Tanzania na Misri la Utalii, Biashara na Uwekezaji na kueleza kuwa Tanzania imeongeza biashara ya mifugo na mazao ya mifugo katika Mfumo wa Stakabadhi za Ghala kwa kuwa unazingatia uwazi, ubora na uaminifu katika biashara.

Akizungumza katika jukwaa hilo (Tanzania–Egypt Tourism, Trade and Investment Forum) lililofanyika nchini Misri na kuwakutanisha wadau wa biashara, uwekezaji na utalii, Bangu amesema mfumo unaotumika kusimamia biashara ya mazao ya kilimo sasa uko tayari kuhudumia pia sekta ya mifugo.

Akifafanua ufanisi wa matumizi ya mfumo huo katika moja ya mijadala iliyokuwepo kwenye jukwaa hilo, Bangu amesema wamefanya kikao kifupi na ujumbe wa Misri ambao wameonesha nia kubwa ya kufanya biashara ya mifugo na bidhaa zitokanazo na mifugo kutoka Tanzania.

“Tunawakaribisha wafanyabiashara wa Misri kuja kufanya biashara Tanzania. Mfumo wetu wa Stakabadhi za Ghala ni wa kuaminika na umejengwa kuhakikisha biashara inafanyika kwa uwazi na usalama kwa pande zote,” amesema.

Amesisitiza kuwa ushirikiano kati ya Tanzania na Misri katika biashara ya mifugo na mazao mengine unaweza kuongeza thamani ya biashara kati ya nchi hizo mbili na kuwanufaisha wazalishaji, wafanyabiashara na uchumi wa Taifa kwa ujumla.

Awali, amefafanua kuwa WRRB haihusiki na hatua ya uzalishaji wa mazao bali huingia baada ya uzalishaji kukamilika kwa kusimamia mnyororo wa biashara unaohakikisha bidhaa zinahifadhiwa, zinakaguliwa na kuuzwa kwa kuzingatia viwango vinavyotakiwa.

Bangu amesema kwa sasa WRRB inashirikiana na Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA), vyama vya ushirika pamoja na wafanyabiashara binafsi katika kuwezesha biashara ya mazao kupitia maghala yaliyosajiliwa na kusimamiwa kisheria.

Ameeleza kuwa bidhaa zinazopelekwa kwenye maghala hayo hukaguliwa ubora na kiasi chake na wataalamu mbalimbali kabla ya kuingizwa katika mfumo rasmi wa biashara.

“Maghala haya yanamilikiwa na sekta binafsi, vyama vya ushirika au Serikali, lakini yote husajiliwa na kusimamiwa na WRRB ili kuhakikisha yanazingatia viwango vinavyotakiwa,” amesema.

Kwa mujibu wa Bangu, mfumo huo unahusisha wataalamu wa ukaguzi wa ubora, usimamizi wa taarifa na ufuatiliaji wa bidhaa kuanzia zilikotoka hadi zinapowekwa ghalani, jambo linaloongeza uaminifu kwa wanunuzi wa ndani na nje ya nchi.

Ameongeza kuwa hatua ya mwisho ni kuandaliwa kwa taarifa kamili za bidhaa husika (catalogue) ambazo huwapatia wafanyabiashara taarifa muhimu kabla ya kufanya maamuzi ya ununuzi.

Bangu amesema WRRB pia inashirikiana na Soko la Bidhaa Tanzania (TMX) kupitia mfumo wa kidijitali unaowezesha wafanyabiashara kutoka sehemu mbalimbali duniani kuona bidhaa zilizopo maghalani na kufanya biashara kwa urahisi.




Na Oscar Assenga,TANGA.
'
Zaidi ya wananchi 20,000 kutoka kaya masikini mkoani Tanga wameanza kunufaika na mpango wa Bima ya Afya kwa Wote, unaolenga kuboresha upatikanaji wa huduma za matibabu kwa kaya zenye kipato cha chini.

Mpango huo, unaotekelezwa kwa awamu ya kwanza na ya pili, unalenga kuwafikia wananchi walio katika mazingira magumu kiuchumi ili kuwawezesha kupata huduma za afya bila kikwazo cha gharama za matibabu. Ufadhili wa mpango huo unatolewa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF), ukiwa na lengo la kupunguza mzigo wa gharama za matibabu kwa kaya masikini.

Hadi sasa, zaidi ya wanufaika 20,000 kutoka kaya 7,816 wamepatiwa kadi za bima ya afya na wameanza kutumia huduma hizo tangu Machi mwaka huu. Hatua hiyo imeelezwa kuwa imeleta matumaini mapya kwa wananchi wengi ambao hapo awali walikabiliwa na changamoto ya kumudu gharama za matibabu.

Akizungumza katika Maonesho ya Kibiashara ya Mwahako, Daktari Lawi Kupaza kutoka Mfuko wa Bima ya Afya (NHIF) Mkoa wa Tanga amesema mwitikio wa wananchi umekuwa mkubwa, huku wengi wa walengwa waliostahili tayari wakikabidhiwa kadi zao.

Amesema zoezi hilo linaendelea vizuri katika halmashauri zote za mkoa huo, huku awamu ya pili ikitarajiwa kufikia kaya nyingine 1,300.

“Kwa sasa tunaendelea na ugawaji wa kadi pamoja na uhakiki wa taarifa za wanufaika. Tunawahamasisha wananchi kujitokeza kuhakiki taarifa zao ili waweze kupata huduma kwa wakati,” amesema Dkt. Kupaza.



Hata hivyo, amekiri kuwepo kwa changamoto ya kuwafikia wanufaika wote kwa wakati kutokana na ukubwa wa maeneo ya utekelezaji na ratiba za shughuli mbalimbali.

“Kuna changamoto ya kuwafikia wanufaika wote kwa wakati kutokana na ratiba na ukubwa wa eneo la utekelezaji. Hata hivyo, watendaji wa kata na vijiji wanaendelea kusaidia katika uhamasishaji,” ameongeza.



Kwa upande wake, Afisa Madai wa NHIF, Neema Kisinga, ameitaka jamii kuendelea kujiunga na bima ya afya ili kujikinga na gharama kubwa za matibabu.

Amesema mfuko huo una vifurushi mbalimbali vinavyowezesha wananchi kupata huduma za afya kwa gharama nafuu, ikiwemo kifurushi cha Tarangire ambacho kinatoa huduma za matibabu, vipimo na ushauri wa daktari kwa gharama nafuu kwa mwaka mzima.



“Kuwa na bima ya afya kunapunguza mzigo wa kulipia huduma kila unapougua au kuhitaji matibabu. Hii ni njia bora ya kujilinda na gharama zisizotarajiwa za afya,” amesema Kisinga.

Mpango huo unaendelea kuonekana kama hatua muhimu katika juhudi za Serikali za kuhakikisha wananchi wote, hususan wa kipato cha chini, wanapata huduma bora za afya bila kuathiriwa na changamoto za kifedha.
Na Ashura Mohamed – Arusha

Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amewataka wasomi na watafiti nchini kuja na suluhisho la kudumu la kumaliza ugonjwa wa Malaria, kama ambavyo wasomi katika mataifa mengine wamefanikiwa kuutokomeza ugonjwa huo.

Akizungumza Jijini Arusha wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa 33 wa Kisayansi wa Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR), Waziri Mchengerwa alisema wataalamu ni lazima waje na tafiti mbalimbali zitakazosaidia jamii kuondokana na changamoto za kiafya.

“Ndugu zangu watafiti, ugonjwa wa Malaria ni lazima sasa ifike mwisho. Wapo wanaotumia dawa lakini haziwasaidii, lakini mazingira yao yapoje? Wapo wanaotumia vyandarua, lakini je watavitumia mpaka maeneo ya kutafuta biashara zao? Hilo si kweli. Au tutatumia njia gani na utaalam gani kumaliza mazalia ya mbu katika mazingira yao? Wajibu wa watafiti ni kuleta suluhisho. Au tukibuni suluhisho taasisi zetu zitakosa kipato? Tuambizane tu,” alisema Mchengerwa.

Aidha, Waziri Mchengerwa alisema haiwezekani changamoto ya Malaria ambayo imedumu kwa miaka zaidi ya mia moja bado iendelee kusumbua nchi zinazoendelea, wakati katika mataifa makubwa duniani ugonjwa huo umekwisha na kuwa historia licha ya kuanzia katika mataifa hayo.

“Ni vema tukakubaliana kuwa maamuzi magumu mtayatafiti katika kipindi hiki. Nikiwa Waziri, tutamshauri Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuyatekeleza ili ugonjwa wa Malaria utokomezwe kabisa. Haiwezekani kila siku tunalia Malaria wakati kuna mataifa Malaria kwao ni historia. Twende tukaokoe vifo vya mama na watoto wachanga chini ya miaka mitano kwa kutokomeza ugonjwa wa Malaria,” alisisitiza Waziri.

Pia alisema anaamini NIMR ikiwezeshwa itapiga hatua katika tafiti mbalimbali, kwa kuwa yapo maeneo yanayoweza kusubiri ila si tafiti.

Alibainisha kuwa mara nyingi fedha zinazotengwa kwa ajili ya tafiti haziwafikii kwa wakati, hali inayokwamisha maendele huku akisisitiza kuwa ili taifa lipige hatua, utafiti haukwepeki.

“Eneo la tafiti kwenye nchi yetu halikwepeki. Tukifanikiwa kwenye tafiti na wenzetu wa mipango wakitusaidia kutafsiri, nchi itapiga hatua kubwa sana, kwa kuwa changamoto zilizopo kwenye jamii zitapata majibu,” alisema.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Taasisi ya Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu(NIMR), Profesa Aboud alisema taasisi hiyo imeendelea kufanya tafiti zinazotegemea ushahidi wa kisayansi na kusaidia uundaji wa sera bora za afya.

Alitaja tafiti zilizochangia mabadiliko ya sera ya chanjo ya saratani ya shingo ya kizazi kutoka dozi mbili hadi dozi moja, pamoja na tafiti za kifua kikuu zinazoonesha uwezekano wa kupunguza muda wa matibabu kutoka miezi sita hadi miezi minne kwa manufaa ya Serikali na wagonjwa.
Waziri wa Afya Mohamed Mchengerwa akizungumza na Watafiti katika Kongamano la 33 la Kisayansi lilioanza Leo Mkoani Arusha


Na Janeth Raphael MichuziTv 

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI, kupitia kwa Mwenyekiti wake Johanes Lukumay, ameipongeza Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) kwa mafanikio makubwa katika utoaji wa huduma za kibingwa na ubobezi, akisema hospitali hiyo imeendelea kuwa tegemeo muhimu kwa wananchi wanaohitaji matibabu ya kiwango cha juu nchini.

Lukumay ametoa pongezi hizo baada ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI kufanya ziara katika hospitali hiyo jijini Dodoma, ambapo ilikagua maendeleo ya ujenzi wa Jengo la Matibabu ya Saratani, kutembelea wagonjwa pamoja na kujionea huduma mbalimbali zinazotolewa na hospitali hiyo.

Akizungumza baada ya ziara hiyo, Lukumay amesema uongozi wa BMH chini ya Mkurugenzi Mtendaji, Profesa Abel Makubi, umeonyesha mfano wa uongozi bora kwa kuhakikisha wananchi wanapata huduma za afya zenye ubora wa hali ya juu.

“Hospitali hii ilianza kutoa huduma za upandikizaji wa uloto mwaka 2023. Hadi sasa watoto 30 tayari wamefanyiwa huduma hiyo kwa mafanikio, jambo ambalo linaonyesha uwezo mkubwa wa kitaalamu uliopo hapa,” alisema Lukumay.

Ameongeza kuwa kati ya watoto hao 30, watoto 20 walipatiwa gharama za matibabu kupitia msaada wa Samia Suluhu Hassan, hatua aliyosema imechangia kwa kiasi kikubwa mafanikio ya huduma hiyo muhimu kwa watoto wenye mahitaji maalum ya matibabu.

“Tunapaswa kuipongeza Hospitali ya Benjamin Mkapa kwa kazi kubwa inayofanya katika kuokoa maisha ya Watanzania na kuendelea kupanua huduma za kibingwa na ubobezi,” alisisitiza.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Afya, Florence Simizi, alimpongeza Rais Samia kwa uwekezaji mkubwa unaoendelea kufanyika katika hospitali hiyo, ambao umeiwezesha kuimarisha huduma za afya kwa wananchi.

Amesema kuelekea maadhimisho ya miaka 10 tangu kuanzishwa kwa hospitali hiyo, serikali imeendelea kushuhudia mafanikio makubwa katika utoaji wa huduma za afya.

“Tumekuja kujionea maendeleo yaliyopo hapa. Hospitali hii kwa sasa inatoa huduma 20 za kibingwa na huduma 17 za ubobezi. Hili si jambo dogo kwa sababu huduma hizi zinahitaji wataalamu wa kada mbalimbali pamoja na miundombinu ya kisasa,” alisema Dkt. Simbazi.

Ameongeza kuwa utoaji wa huduma hizo unategemea uwepo wa miundombinu bora, vifaa tiba vya kisasa na wataalamu wenye ujuzi wa hali ya juu, mambo ambayo yameendelea kupewa kipaumbele na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa BMH, Profesa Makubi, amesema hospitali hiyo inaendelea kutekeleza mipango mbalimbali ya maendeleo yenye lengo la kuifanya kuwa kituo kikuu cha matibabu nchini.

Amesema moja ya maono ya hospitali hiyo ni kuona BMH ikifikia hadhi ya Hospitali ya Taifa, huku maeneo ya wazi yanayozunguka hospitali yakitumika kuanzisha “Kijiji cha Matibabu” kitakachojumuisha huduma mbalimbali za afya na uwekezaji katika sekta ya tiba.

Profesa Makubi ameeleza kuwa hatua hiyo itachochea maendeleo ya sekta ya afya, kuongeza upatikanaji wa huduma za kibingwa na ubobezi, pamoja na kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha huduma za matibabu katika ukanda wa Afrika Mashariki.












Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Dkt. Jabiri K. Bakari, amewataka watumishi wa Mamlaka hiyo kuendana na mabadiliko kwa kujenga utamaduni wa kupanga, kubuni, kushirikiana na kuwahusisha wadau katika utekelezaji wa majukumu yao, akieleza kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kuimarisha utendaji wa taasisi na kuchochea maendeleo endelevu ya sekta ya usafiri wa anga nchini.

Dkt. Bakari alitoa rai hiyo wakati wa mafunzo maalum ya siku nne yaliyofanyika katika Chuo cha Uongozi cha Mwalimu Julius Nyerere, Kibaha, kuanzia Juni 5 hadi 8, yaliyowakutanisha viongozi na wawakilishi wa watumishi wa TCAA kutoka vituo mbalimbali nchini.

Mafunzo hayo yalitoa fursa kwa washiriki kutafakari utendaji wa Mamlaka, kujadili vipaumbele vya kimkakati na kubaini njia bora za kuimarisha utoaji wa huduma pamoja na ufanisi wa taasisi kwa ujumla.

Sehemu ya kwanza ya mafunzo ilijikita katika maendeleo binafsi na ujenzi wa timu kupitia programu iliyoendeshwa na Peak Performance. Kupitia shughuli mbalimbali za ndani na nje ya darasa, washiriki walishiriki mazoezi yaliyolenga kuimarisha mshikamano, kujenga kuaminiana, kuboresha mawasiliano na kuhamasisha mabadiliko chanya ya fikra na mtazamo.

Washiriki walihamasishwa kutafakari upya namna wanavyotekeleza majukumu yao, kujenga nidhamu binafsi, kuzingatia afya na ustawi wa mwili pamoja na kuendeleza tabia zinazochangia mafanikio ya mtu mmoja mmoja na taasisi kwa ujumla. Mafunzo hayo pia yalisisitiza umuhimu wa kujitambua, uwajibikaji na kuwa na mtazamo chanya katika kufanikisha malengo ya pamoja.

Moja ya matokeo muhimu ya mafunzo hayo ilikuwa kuandaliwa kwa waraka wa pamoja wa kujenga timu (Team Building Charter) unaoakisi maadili, matarajio na dhamira ya pamoja iliyojengwa wakati wa mafunzo hayo. Waraka huo unatarajiwa kuwa mwongozo wa kuimarisha utamaduni wa taasisi, kukuza ushirikiano na uwajibikaji, pamoja na kusaidia juhudi za Mamlaka katika kufikia ubora wa utendaji na utoaji huduma.

Katika kipindi chote cha mafunzo, washiriki pia walijadili masuala mbalimbali ya kimkakati ikiwemo utendaji wa Mamlaka, mipango ya bajeti, michakato ya kazi, ushirikishwaji wa wadau na fursa za kuboresha utoaji wa huduma. Majadiliano hayo yalitoa nafasi kwa viongozi na watumishi kutathmini changamoto zilizopo, kubaini fursa na kujadiliana kuhusu suluhisho zitakazosaidia kuimarisha ufanisi wa Mamlaka.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, Dkt. Bakari alisisitiza umuhimu wa kuondokana na utamaduni wa kushughulikia matatizo baada ya kutokea na badala yake kujenga utamaduni wa kupanga, kufanya tafiti na kufanya maamuzi kwa kuzingatia taarifa sahihi na ushahidi.

Aliwataka watumishi kutumia tafiti, takwimu na taarifa za wakati halisi katika kuelewa mwenendo wa sekta na kufanya maamuzi yatakayosaidia kuimarisha huduma na kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa majukumu ya Mamlaka.

Mkurugenzi Mkuu huyo pia alisisitiza umuhimu wa kuzingatia dhana ya “Know Your Customer” (KYC) kwa kuwafahamu kwa kina wadau wa sekta ya anga, kuelewa mahitaji yao na kujenga mahusiano mazuri yatakayowezesha utoaji wa huduma bora zaidi.

“Lazima tuwafahamu wateja na wadau wetu, tuelewe changamoto zao na mazingira wanayofanyia kazi. Uelewa mzuri wa wadau wetu utatuwezesha kufanya maamuzi sahihi, kuboresha utoaji wa huduma na kuchangia kwa ufanisi maendeleo ya sekta ya usafiri wa anga,” alisema.

Dkt. Bakari alisisitiza pia umuhimu wa kujenga na kuendeleza mahusiano imara na wadau mbalimbali wa sekta ya anga, akieleza kuwa ushirikiano, kuaminiana na mawasiliano endelevu ni nguzo muhimu katika kuhakikisha sekta hiyo inaendelea kukua kwa usalama, ufanisi na ushindani.

Aidha, aliwataka watumishi kufuatilia kwa karibu mwenendo wa sekta, kufanya tafiti na kutumia taarifa mbalimbali katika kuelewa changamoto na mahitaji ya wadau ili kusaidia kufanya maamuzi yenye tija kwa maendeleo ya sekta.

Kwa upande mwingine, Dkt. Bakari alisisitiza umuhimu wa afya na ustawi wa watumishi, akibainisha kuwa taasisi yenye watumishi wenye afya njema, ari ya kazi na mtazamo chanya ndiyo yenye uwezo mkubwa wa kufanikisha malengo yake. Aliwahimiza watumishi kuzingatia afya zao za mwili na akili ili kuwa na nguvu na uthabiti wa kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Mafunzo hayo yalihitimishwa kwa washiriki kubaini suluhisho za changamoto mbalimbali za kiutendaji na kuthibitisha upya dhamira yao ya kuimarisha ushirikiano, ubunifu, ushirikishwaji wa wadau na utoaji wa huduma bora.

Majadiliano yaliyofanyika yanaakisi dira ya TCAA ya kujenga taasisi yenye utendaji wa hali ya juu inayoweza kuendelea kuisimamia na kuiendeleza sekta ya usafiri wa anga kwa usalama, ufanisi na kwa kuzingatia mahitaji ya wadau wake.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Dkt. Jabiri K. Bakari akizungumza wakati wa mafunzo maalum ya siku nne ya kuimarisha utendaji wa taasisi na kuchochea maendeleo endelevu ya sekta ya usafiri wa anga nchini yaliyofanyika katika Chuo cha Uongozi cha Mwalimu Julius Nyerere, Kibaha mkoani Pwani.






Baadhi ya watumishi wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) wakiwa kwenye mafunzo ya kuimarisha utendaji wa Taasisi hiyo.

WAZIRI wa Viwanda na Biashara Judith Kapinga, amesema Serikali imeendelea kuweka mazingira bora ya uwekezaji na biashara kwa kuboresha sera, sheria na mifumo ya utoaji huduma kuvutia uwekezaji wenye tija.

Kapinga ameyasema hayo jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa chapa mpya ya magari Jetour, jijini Dar es Salaama, ambapo amefafanua uzinduzi huo unaendana kikamilifu na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mpango wa Tatu wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano na Ajenda ya Taifa ya Ujenzi wa Uchumi wa Viwanda na Biashara.

Ameongeza uwekezaji huo unadhihirisha dhamira ya kukuza ushiriki wa sekta binafsi, kuongeza matumizi ya rasilimali za ndani,uhamishaji wa teknolojia na kuzalisha ajira kwa Watanzania.

"Tunatambua Africarriers na Jetour hawaleti magari pekee nchini bali wanaleta fursa mpya za biashara, uwekezaji, ajira, maarifa ya kiteknolojia na mchango mkubwa katika maendeleo ya uchumi wa Tanzania na ukanda wetu wa Afrika Mashariki,”amesema Waziri Kapinga.

Pia amewapongeza viongozi wa Africarriers Group na Jetour Global kwa maono yao makubwa kuichagua Tanzania kuwa sehemu ya safari yao ya ukuaji na mafanikio huku akisisitiza Serikali itaendelea kushirikiana na wawekezaji wote wenye nia ya dhati ya kuchangia maendeleo ya Taifa letu.

Akieleza zaidi amesema ujio wa Jetour nchini Tanzania kunafungua ukurasa mpya wa fursa za kiuchumi na uwekezaji huo utazalisha ajira mpya kwa vijana katika maeneo mbalimbali yakiwemo ya mauzo, huduma za kiufundi, ushauri wa huduma kwa wateja, teknolojia ya habari na mawasiliano pamoja na huduma nyingine.

Waziri Kapinga amesema pia mafanikio ya Africarriers kwa kipindi cha zaidi ya miaka 50 ni ushahidi wa uwezo, uthubutu na ustahimilivu wa wafanyabiashara wa Kitanzania.

“Kupitia ushirikiano huo na Jetour, watapiga hatua nyingine muhimu kuelekea Tanzania yenye viwanda imara, ajira nyingi, biashara shindani na uchumi jumuishi kwa kizazi cha sasa na vizazi vijavyo.”

Kwa upande wa Mkuu wa Idara ya Sheria wa Kampuni za Africarries, Ngasa Mboje amesema kwa mara ya kwanza wameleta gari zinazoendana na soko na mahitaji ya Watanzania kwasababu ni gharama nafuu.

“Magari ya Jetour yanauzwa kwa njia ya malipo ya papo kwa hapo na njia ya mpili ni kwa mkopo kwasababu kuna baadhi ya Watanzania hawawezi kumudu gharama kwa mara kwanza.Hivyo unaweza kununua kwa mkopo na kulipa kidogo kidogo, huku ukiendelea kulitumia gari lako.”
Mgeni rasmi Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe.Judidh Salvio Kapinga akizungumza mbele ya Wageni waalikwa mbalimbali waliofika kwenye hafla ya uzinduzi rasmi wa Chapa mpya ya Magari ya Jetour nchini Tanzania,iliofanyika Juni 8,2026 Masaki, jijini Dar es Salaam

Balozi wa Shirikisho la Urusi nchini Tanzania Mhe. Andrey Avetisyuan akizungumza mbele ya Wageni waalikwa mbalimbali waliofika kwenye hafla ya uzinduzi rasmi wa Chapa mpya ya Magari ya Jetour nchini Tanzania,iliofanyika Juni 8,2026 Masaki, jijini Dar es Salaam,ambapo mgeni rasmi alikuwa ni Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe.Judidh Salvio Kapinga
Makamu wa Rais wa Kampuni ya Magari ya Africarriers Group,Bw. Shahid Nabi, akizungumza mbele ya Wageni waalikwa mbalimbali waliofika kwenye hafla ya uzinduzi rasmi wa Chapa mpya ya Magari ya Jetour nchini Tanzania,iliofanyika Juni 8,2026 Masaki, jijini Dar es Salaam,ambapo mgeni rasmi alikuwa ni Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe.Judidh Salvio Kapinga
Baadhi ya Viongozi na wageni waalikwa wakishuhudia uzinduzi wa Chapa mpya ya Magari ya Jetour nchini Tanzania,hafla iliofanyika Juni 8,2026 Masaki, jijini Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa Makampuni ya Africarriers, Bw. Fida Rashid, akimkabidhi Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania, Mhe. Chen Mingjian mfano wa gari ya Jetour iliozinduliwa nchin Tanzania.
Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania, Mhe. Chen Mingjian akiwasha gari ya Jetour iliozinduliwa nchini Tanzania hapo jana,Masaki jijini Dar es Salaam.
Picha ya pamoja mara baada ya uzinduzi wa Chapa mpya ya Magari ya Jetour nchini Tanzania,hafla iliofanyika Juni 8,2026 Masaki, jijini Dar es Salaam.





Top News