Na Janeth Raphael - MichuziTv
Katika kuimarisha juhudi za kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini, waandishi wa habari na maafisa mawasiliano Serikalini wamehimizwa kujenga ushirikiano wa karibu na wadau mbalimbali ili kuongeza ufanisi wa utoaji wa elimu na utekelezaji wa kampeni zinazolenga kufikisha ujumbe kwa wananchi.
Wito huo umetolewa na Mshauri wa Mawasiliano kutoka Kampuni ya Kengo, Niwaeli Gittens-Mbaga, wakati akiwasilisha mada kuhusu nafasi ya vyombo vya habari katika kuendeleza ajenda ya nishati safi ya kupikia kwenye siku ya pili ya warsha ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari pamoja na maafisa mawasiliano kutoka mikoa, wizara na taasisi mbalimbali za Serikali inayofanyika mkoani Morogoro.
Katika mada yake, Gittens-Mbaga alieleza kuwa mafanikio ya kampeni za nishati safi ya kupikia yanategemea kwa kiwango kikubwa uwezo wa wadau wa mawasiliano kuanzisha na kudumisha mahusiano yenye tija na taasisi, washirika wa maendeleo pamoja na sekta binafsi zinazoweza kuchangia rasilimali na utaalamu.
Aidha, aliwapa washiriki mbinu za kuandaa mapendekezo ya miradi (project proposals) yanayokidhi mahitaji ya wadau mbalimbali, akisisitiza umuhimu wa kuzingatia vipaumbele na maslahi ya kila mdau ili kuongeza nafasi ya kupata ushirikiano na ufadhili wa utekelezaji wa miradi ya kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia.
Baada ya sehemu ya nadharia, washiriki walishiriki mazoezi ya vitendo kwa kugawanywa katika makundi tofauti, ambapo kila kundi liliandaa pendekezo la mradi wa mawasiliano kuhusu nishati safi ya kupikia na kuliwasilisha mbele ya wawezeshaji pamoja na washiriki wengine.
Uwasilishaji huo uliambatana na mjadala na mrejesho wa kitaalamu uliolenga kuboresha ubora wa mapendekezo hayo, huku washiriki wakipata fursa ya kuimarisha uelewa wao kuhusu mbinu bora za kushirikisha wadau na kutumia mawasiliano yenye matokeo katika kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.
Warsha hiyo inaendelea kuwajengea washiriki uwezo wa kitaalamu ili kuwawezesha kuandaa na kusambaza maudhui sahihi yatakayochochea uelewa wa jamii na kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali kufikia malengo ya ajenda hiyo nchini.
.jpeg)
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, ambaye pia ni Msarifu wa Taasisi ya Benjamin William Mkapa Foundation, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema njia bora ya kuuenzi urithi wa Hayati Rais Benjamin William Mkapa ni kuendelea kuwekeza katika uongozi, kuimarisha mifumo ya afya na kuwawezesha vijana kuwa wasanifu wa mustakabali wa Afrika.
Rais Dkt. Mwinyi amesema hayo leo, tarehe 16 Julai 2026, katika Jukwaa la Nne la Kuuenzi Urithi wa Mkapa pamoja na Maadhimisho ya Miaka 20 tangu kuanzishwa kwa Taasisi ya Benjamin William Mkapa Foundation, yaliyofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC), jijini Dar es Salaam.
Amesema Taasisi ya Benjamin William Mkapa Foundation imeendelea kuwa mshirika muhimu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha mifumo ya afya, kuendeleza rasilimali watu wa sekta ya afya na kuboresha huduma za afya ya msingi kwa wananchi.
Katika hafla hiyo, Rais Dkt. Mwinyi alitunukiwa Tuzo Maalumu ya kutambua mchango wake katika maendeleo ya Taasisi ya Benjamin William Mkapa Foundation, iliyokabidhiwa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Emmanuel John Nchimbi.
Aidha, Rais Dkt. Mwinyi alimkabidhi Mhe. Dkt. Nchimbi Tuzo ya Juu ya Uongozi katika Mageuzi ya Afya kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Emmanuel John Nchimbi, Mama Anna Mkapa, Viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mabalozi, Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika, Prof. Mohamed Yakub Janabi, wawakilishi wa Taasisi za kimataifa, Wadau wa maendeleo, wataalamu wa afya na Wageni mbalimbali waalikwa.
MAMLAKA ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira mjini Moshi (MUWSA) imeendelea na jitihada zake za kuhakikisha upatikanaji wa maji katika kata ya Marangu Mashariki wilayani Moshi mkoani Kilimanjaro unakuwa ni wa uhakika ambapo wameendelea kuboresha miundombinu kwa kununua mabomba mapya ya kulaza umbali wa kilomita 13.
Akizungumza mara baada ya kuwasili kwa mabomba hayo, Mkuu wa Idara ya Ufundi, Mhandisi Innocent Lugodisha alisema kuwa, mradi huo unatekelezwa kwa awamu mbili ambapo mamlaka tayari imeshakamilisha awamu ya kwanza ya mradi.
Mhandisi Lugodisha alisema kuwa, mradi huo unatarajiwa kugharimu shilingi 1,470,121,709 ambapo awamu ya kwanza 234,355,900 na awamu ya pili utatumia 1,235,765,808.
"Mradi huu ukikamilika utasaidia upatikanaji wa maji katika vijiji vya Samanga, Rauya na Ashira kuwa wa uhakika ambapo utaongeza uzalishaji maji kutoka mita za ujazo 402 hadi 4320 kwa siku na mahitaji kwa vijiji hivi ni mita za ujazo 1164" alisema Mhandisi Lugodisha.
Alisema kuwa, awamu ya kwanza ulihusisha ujenzi wa chanzo cha Lyasongoro na Kyerio, ujenzi wa uzio katika chanzo, ujenzi wa break pressure na ulazaji wa bomba zenye urefu wa kilomita 2.4.
Aliongeza kuwa, katika awamu ya pili kazi zitakazoenda kufanyika ni uchimbaji wa mtaro na ulazaji wa bomba lenye kipenyo cha inchi 8 na 6 lenye urefu wa kilomita 13.
Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Vunjo, Enock Koola alisema kuwa, mradi huo utakapokamilika utasaidia kuondoa tatizo la maji kabisa katika vijiji vya Rauya, Samanga na Ashira ambavyo vilikuwa vikipata maji chini ya asilimia 50.
"Wakati wa ziara ya Waziri Mkuu mkoani Kilimanjaro niliwasilisha changamoto ya upatikanaji maji katika jimbo letu hususani kata hii ya Marangu mashariki na Waziri Mkuu alimwagiza Waziri wa maji kuhakikisha upatikanani maji kwa wananchi unatatuliwa na aliahidi kulitatua ndani ya muda mfupi na matokeo yameanza kuonekana kupitia mradi huo" alisema Koola.
Na Mwandishi wetu, Mirerani
MWENGE wa uhuru umekagua na kutembelea mradi wa viti 120 na meza 120 za wanafunzi wa shule ya sekondari Tanzanite ya Kata ya Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara.
Mkuu wa shule ya sekondari Tanzanite, Jude Samwel Mziray ameeleza hayo wakati akisoma taarifa ya mradi huo kwa kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru mwaka 2026 Wazo Mwang'onda.
Mwalimu Mziray amesema shule ya sekondari Tanzanite ilipokea viti na meza hizo Mei 28, mwaka 2026.
Amesema shule hiyo ilipokea viti 120 na meza 120 kwa ajili ya maandalizi ya kuwapokea wanafunzi wa kidato cha kwanza 2028 watakaohitimu darasa la sita na la saba kwa wakati mmoja 2027.
"Mradi huu umezingatia kigezo namba 53 cha namna Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro ilivyoandaa miundombinu ya kupokea wanafunzi wa kidato cha kwanza mwaka 2028," amesema.
Amesema mradi huo umetengewa kiasi cha shilingi 10,800,000.00 kutoka katika mapato ya Halmashauri ya Wilaya na fedha iliyotumika ni shilingi 10,560,000.00
"Ndugu kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru kitaifa mradi huu umetekelezwa kwa kutumia mfumo wa kielektroniki wa manunuzi ya Taifa (NaST) na fundi aliyetengeneza viti 120 na meza 120 ni Ibrahim Elias Mmary.
Amesema mafanikio ya mradi huo wa viti na meza ni kupunguza idadi ya wanafunzi wasiokuwa na viti na meza watakaoingia kidato cha kwanza 2028 na vyumba vitatu kuanza kutumika.
"Tunaishukuru Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuboresha mazingira ya kujisomea na kujifunzia katika shule hii," amesema mwalimu Mziray.
Hata hivyo, kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru kitaifa mwaka 2026 amepongeza mradi huo ambao utakuwa na manufaa makubwa kwa wanafunzi hao.
Mwang'onda amewaasa wanafunzi wa shule hiyo watakaotumika madawati na meza hizo kuzitunza ili waweze kutumia kwa muda mrefu.
Sekta ya mifugo nchini inatarajiwa kuingia katika hatua mpya ya utoaji wa huduma kufuatia kuanzishwa kwa zana za kidijitali za Mfumo wa Ulezi wa Kitaaluma kwa Maduka ya Dawa za Mifugo (Agrovet Mentoring Framework–AMF) na Mfumo wa Ulezi wa Kitaaluma kwa Watoa Huduma za Afya ya Mifugo (Animal Health Mentoring Framework–AHMF), ambazo zinalenga kuongeza ubora, uwajibikaji na weledi katika sekta hiyo.
Akizungumza katika kikao cha wadau kilichowakutanisha taasisi mbalimbali za sekta ya mifugo Jijini Dodoma, Msajili wa Baraza la Madaktari wa Mifugo Tanzania, Dkt. Amani Kilemile, alisema mfumo wa sasa unaotumia nyaraka za karatasi katika kufuatilia na kusimamia wataalamu wa mifugo pamoja na wahudumu wa maduka ya dawa za mifugo umekuwa ukikabiliwa na changamoto mbalimbali, zikiwemo ugumu wa kufuatilia utendaji wa wataalamu, kuhifadhi kumbukumbu sahihi na kusimamia uzingatiaji wa viwango vya taaluma.
Alisema matumizi ya zana hizo za kidijitali yatamwezesha mlezi wa kitaaluma kufanya tathmini ya umahiri wa mtaalamu kwa wakati halisi, kurekodi maendeleo yake na kutoa mrejesho wenye muundo unaoeleweka, hatua itakayoongeza uwajibikaji na kuboresha ubora wa huduma zinazotolewa kwa wafugaji.
Dkt. Kilemile aliongeza kuwa tofauti na mfumo wa awali wa karatasi, zana hizo zitamwezesha mlezi kushuhudia utendaji wa kila siku wa mtaalamu, kubaini mapungufu ya uwezo, kutoa mafunzo ya vitendo na kufuatilia maendeleo yake kwa karibu ili kuhakikisha viwango vya kitaaluma vinaendelea kuzingatiwa.
Alisema mifumo hiyo pia itasaidia kusimamia maeneo muhimu ikiwemo uzingatiaji wa sheria na kanuni za taaluma, utoaji bora wa huduma kwa wateja, usambazaji unaowajibika wa dawa za mifugo, usimamizi wa stoo za dawa na bidhaa za mifugo pamoja na kuimarisha maadili ya taaluma.
Zana hizo zimetengenezwa na Brooke East Africa, shirika la ustawi wa wanyama lenye makao yake nchini Kenya, na zinatekelezwa nchini Tanzania na INADES-Formation Tanzania kwa kushirikiana na Arusha Society for Protection of Animals (ASPA), kwa lengo la kujenga uwezo wa wataalamu wa afya ya mifugo na wahudumu wa maduka ya dawa za mifugo.
Kwa upande wake, Wizara inayosimamia sekta ya mifugo ilieleza kuwa mfumo huo wa kidijitali utarahisisha ukusanyaji na uchambuzi wa taarifa, kuongeza ufanisi wa usimamizi na kuwezesha maamuzi yanayotegemea ushahidi, tofauti na mfumo wa karatasi ambao umekuwa ukisababisha ucheleweshaji wa taarifa na changamoto za ufuatiliaji.
Mkurugenzi Mtendaji wa INADES-Formation Tanzania, Bi. Jacqueline Nicodemus, pamoja na wawakilishi wa ASPA na Brooke East Africa, walisisitiza dhamira yao ya kuendelea kushirikiana na Serikali kuhakikisha mifumo hiyo inatekelezwa kwa ufanisi ili kuleta mageuzi katika sekta ya mifugo.
Wadau walieleza matumaini kuwa matumizi ya mifumo ya AMF na AHMF yataongeza uwezo wa wataalamu wa mifugo, kuboresha afya na ustawi wa wanyama, kuongeza uzalishaji wa mifugo, kuhamasisha matumizi sahihi ya dawa za mifugo na kujenga imani zaidi kwa wafugaji kupitia huduma zenye ubora, weledi na uwajibikaji.
MWENYEKITI wa Mtaa wa Mwime, Manispaa ya Kahama mkoani Shinyanga, Stella Bhayugile, amesema utekelezaji wa miradi ya maendeleo pamoja na mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na Serikali inayoongozwa na Rais Dk Samia Suluhu Hassan umeendelea kuleta matumaini mapya kwa wananchi.
Huku vijana na wanawake wakinufaika kwa kiwango kikubwa kupitia vikundi vyao vya uzalishaji na ujasiriamali.
Akizungumza katika mahojiano maalumu ofisini kwake Jumatano, Julai 15, 2026, Bhayugile alisema Mtaa wa Mwime unaendelea kushuhudia maendeleo makubwa yanayochochewa na usimamizi mzuri wa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Alisema kupitia Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, vikundi zaidi ya 12 vya vijana na wanawake katika mtaa wa Mwime tayari vimepatiwa mikopo inayotokana na asilimia 10 ya mapato ya ndani ya halmashauri, hatua ambayo imewawezesha kuanzisha na kupanua shughuli mbalimbali za kiuchumi.
"Mpaka sasa zaidi ya vikundi 12 vya vijana na wanawake vimepata mikopo katika kipindi cha robo mbili za mwaka wa fedha. Mikopo hii imewapa uwezo wa kujiajiri, kuongeza kipato cha familia na kuboresha maisha yao.
Tunamshukuru sana Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuweka mazingira yanayowainua wananchi kiuchumi," alisema Bhayugile.
Alibainisha uongozi wa mtaa huo umeendelea kushirikiana kwa karibu na wananchi katika kusimamia miradi ya maendeleo ili kuhakikisha fedha zinazotolewa na Serikali zinatumika kwa ufanisi na kuleta matokeo yanayoonekana.
Mbali na mikopo hiyo, Bhayugile alisema Mtaa wa Mwime umefanikiwa kujenga zahanati inayotoa huduma za afya kwa wananchi, hivyo kupunguza adha ya kusafiri umbali mrefu kufuata matibabu.
Aidha, alisema eneo hilo lina shule ya msingi yenye wanafunzi zaidi ya 1,886, huku juhudi zikiendelea kuboresha mazingira ya kujifunzia kupitia ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya elimu.
Alieleza matundu 16 ya vyoo yamejengwa, na kwa sasa unaendelea mradi wa kufumua mfumo wa mashimo ya zamani ili kujenga vyoo vipya vya kisasa vitakavyokidhi mahitaji ya wanafunzi na walimu.
Katika sekta ya miundombinu, Bhayugile alisema Serikali imetoa zaidi ya Sh milioni 15 kwa ajili ya ukarabati wa barabara za Mtaa wa Mwime na maeneo jirani, hatua ambayo imeboresha usafiri na kurahisisha shughuli za kiuchumi kwa wananchi.
Pia alisema Serikali inaendelea kuwekeza katika kuboresha huduma za elimu kwa watoto wenye mahitaji maalumu, wakiwemo wenye ulemavu wa kusikia, uoni hafifu,mtindio wa ubongo na makundi mengine yanayohitaji mazingira rafiki ya kujifunzia.
Bhayugile alisema mafanikio hayo yametokana na ushirikiano mkubwa uliopo kati ya wananchi, viongozi wa Serikali za Mitaa na Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, akisisitiza kuwa maendeleo haya ni ishara ya dhamira ya Serikali ya kuhakikisha hakuna mwananchi anayebaki nyuma.
Aliwataka wananchi kuendelea kushiriki katika shughuli za maendeleo, kulinda miradi inayotekelezwa na kutumia ipasavyo fursa zinazotolewa na Serikali kwa ajili ya kuinua uchumi wa familia na Taifa kwa ujumla.



.jpeg)


.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)

.jpeg)


.jpeg)



.jpeg)



.jpeg)
.jpeg)





.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)
.jpeg)







