OWM-TAMISEMI

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa  (OWM– TAMISEMI) anayeshughulikia masuala ya Afya, Mhe. Dkt. Jafari Seif, amesema kuwa hali ya upatikanaji wa bidhaa za afya katika ngazi ya huduma za afya ya msingi nchini imeendelea kuimarika na kufikia kiwango cha kuridhisha ikilinganishwa na miaka iliyopita.

Akizungumza Aprili 2, 2026 jijini Dar es Salaam, katika kikao kazi kilichoongozwa na Waziri wa Afya, Mhe.Mohamed Mchengerwa, pamoja na wadau wa sekta ya afya, katika ofisi za Bohari ya Dawa (MSD), Mhe. Dkt. Seif amesema kuwa tathmini ya mwaka 2026 inaonesha hali ya upatikanaji wa dawa imefikia asilimia 89 katika hospitali, asilimia 88 katika vituo vya afya, na asilimia 88 katika zahanati.

Ameongeza kuwa katika mwaka wa fedha 2024/25, vituo vya kutolea huduma za afya ngazi ya msingi vilikusanya takribani Shilingi Bilioni 108, huku makusanyo hayo yakitarajiwa kuongezeka hadi kufikia Shilingi Bilioni 192 katika mwaka 2025/26.   

Kwa upande wake, Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amemuelekeza Katibu Mkuu wa wizara hiyo kushirikiana kwa karibu na Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI kuandaa na kusimamia miongozo, taratibu na miundo ya usimamizi wa vituo vya kutolea huduma za afya. Lengo la hatua hiyo ni kuhakikisha kuwa wafamasia kote nchini wanakuwa sehemu muhimu ya timu za menejimenti katika vituo hivyo, ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za afya.






 Na Benny Mwaipaja, Tangier-Morocco


Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar, ametoa wito kwa nchi za Afrika kuwa na mtazamo wa pamoja katika kubuni na kutekeleza mikakati ya muda mfupi, wa kati na mrefu, ambayo ni endelevu na jumuishi, itakayopunguza utegemezi na kuimarisha uthabiti wa uchumi wa Bara la Afrika ili kukabiliana na majanga na migogoro ya vita inayoendelea duniani.

Mhe. Balozi Omar alitoa wito huo jijini Tangier nchini Morocco, katika Mkutano wa 58 wa Mawaziri wa Fedha, Mipango na Maendeleo ya Uchumi na Magavana wa Benki Kuu wa Afrika, wakati akichangia mjadala kufuatia taarifa ya Kamisheni ya Umoja wa Mataifa inayosimamia Uchumi Afrika (UNECA), inayochambua athari za mgogoro unaoendelea Mashariki ya Kati namna ulivyoleta athari hasi za kiuchumi na kijamii katika Bara la Afrika.

Alibainisha kuwa baadhi ya nchi za Afrika, hususan zile zinazotegemea sekta ya utalii, zinaweza kuathirika zaidi na Mgogoro unaoendelea Mashariki ya Kati.

Kwa upande wa Tanzania, alibainisha kuwa Serikali inaendelea kufuatilia kwa karibu mwenendo wa mgogoro huo kupitia ushirikiano katika Wizara za Kisekta na Taasisi zake, ili kubaini hatua stahiki za kisera zitakazolinda ustawi wa uchumi na maslahi ya wananchi.

Vilivile, alieleza kuwa pamoja na kwamba mgogoro huo umeathiri mtiririko wa biashara kwa kuwa ukanda wa Mashariki ya Kati ni lango muhimu la biashara kati ya Afrika na masoko ya kimataifa. Hivyo, ni muda muafaka wa Afrika kuona umuhimu wa kuwa na njia mbadala ya kufanya biashara hususan miongoni mwa nchi wanachama.

Mheshimiwa Balozi Omar alisisitiza kuwa kwa muda mrefu Afrika imekuwa ikijadili umuhimu wa kutumia rasilimali zake ipasavyo, na kwamba hali ya sasa inatoa fursa ya kuchukua hatua madhubuti za kujitegemea kwa kutumia rasilimali zake.

Alifafanua kuwa Bara la Afrika lina rasilimali za kutosha, ikiwemo mafuta na mbolea, ambazo zinaweza kuzalishwa na kupatikana ndani ya Bara kupitia ushirikiano, hususan Eneo Huru la Biashara Barani Afrika (AfCFTA).

Mhe. Balozi Omar alieleza kuhusu umuhimu wa kuendelea na majadiliano chini ya uratibu wa UNECA kuhusu mageuzi katika mifumo inayosimamia maamuzi na sera za kifedha duniani (Global Financial Architecture), ili Afrika iweze kuwa na sauti moja yenye nguvu katika upatikanaji wa rasilimali za kifedha kwa gharama nafuu kwa ajili ya maendeleo endelevu.

Alisisitiza kuwa mafanikio ya mageuzi hayo yatategemea mshikamano na ushirikiano thabiti wa nchi za Afrika.

Baadhi ya Washiriki wa Mkutano huo, walieleza kuwa ili kukabiliana na mizozo hiyo nchi za Afrika zinahitaji kuweka sera na mikakati ya kuondoa vikwazo vya ufanyaji biashara na upitishaji wa bidhaa kwa kufungua mipaka yake.

Aidha, walishauri kuwa umefika wakati wa nchi za Afrika kuzalisha mafuta yake na kutumia vyanzo vingine mbadala vya nishati ili kukabiliana na uhaba wa mafuta na kupanda kwa bidhaa hiyo muhimu katika uzalishaji na uchumi wa mataifa hayo.

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akichangia mjadala kufuatia taarifa ya Kamisheni ya Umoja wa Mataifa inayosimamia Uchumi Afrika (UNECA), iliyochambua athari za mgogoro unaoendelea Mashariki ya Kati namna ulivyoleta athari hasi za kiuchumi na kijamii katika Bara la Afrika na namna ya kukabiliana nazo, katika Mkutano wa 58 wa Mawaziri wa Fedha, Mipango na Maendeleo ya Uchumi na Magavana wa Benki Kuu wa Afrika, unaofanyika jijini Tangier nchini Morocco.







Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akishiriki Mkutano wa 58 wa Mawaziri wa Fedha, Mipango na Maendeleo ya Uchumi na Magavana wa Benki Kuu wa Afrika wa Kamisheni ya Umoja wa Mataifa inayosimamia Uchumi Afrika (UNECA), unaofanyika jijini Tangier nchini Morocco, ambao pamoja na mambo mengine unajadili athari za mgogoro unaoendelea Mashariki ya Kati namna ulivyoleta athari hasi za kiuchumi na kijamii katika Bara la Afrika na namna ya kukabiliana nazo. Mkutano huo umewashirikisha pia Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Mipango na Uwekezaji Mhe. Dkt. Pius Chaya na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba.
(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Tangier-Morocco)



(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini-Wizara ya Fedha, Tangier, Morocco)



Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akichangia mjadala kufuatia taarifa ya Kamisheni ya Umoja wa Mataifa inayosimamia Uchumi Afrika (UNECA), iliyochambua athari za mgogoro unaoendelea Mashariki ya Kati namna ulivyoleta athari hasi za kiuchumi na kijamii katika Bara la Afrika na namna ya kukabiliana nazo, katika Mkutano wa 58 wa Mawaziri wa Fedha, Mipango na Maendeleo ya Uchumi na Magavana wa Benki Kuu wa Afrika, unaofanyika jijini Tangier nchini Morocco.


(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini-Wizara ya Fedha, Tangier, Morocco) 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Alhaj Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesisitiza umuhimu wa kuendelea kulinda na kudumisha amani, umoja na mshikamano nchini, akihimiza wananchi kuondoa ubaguzi na kuimarisha upendo katika jamii.

Amesema umoja wa wananchi ni msingi muhimu wa utulivu wa Taifa, na kila mmoja ana wajibu wa kulinda tunu hizo kwa vitendo.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, Aprili 03, 2026, baada ya kushiriki Sala ya Ijumaa iliyoambatana na Dua Maalum ya kuiombea nchi, viongozi na marehemu, iliyofanyika Msikiti wa Mzee Ali Hassan Mwinyi, Mangapwani.

Dua hiyo imeandaliwa na Ofisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar kwa kushirikiana na Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Juma Malik Akil, na imefanyika katika Msikiti wa Mzee Ali Hassan Mwinyi uliopo Mangapwani, Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Aidha, amewataka waumini kuepuka makundi yenye viashiria vya chuki na migawanyiko, akisisitiza kuwa dini inahimiza amani na uvumilivu.

Dua hiyo imehudhuriwa na Mke wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Mama Mariam Mwinyi, viongozi mbalimbali wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, viongozi wa dini pamoja na ndugu, jamaa na marafiki.

Sambamba na hayo, Rais Dkt.Mwinyi, akiwa ameambatana na viongozi mbalimbali wa Serikali na waumini, walizuru kaburi la Hayati Mzee Ali Hassan Mwinyi kwa ajili ya kumuombea dua maalum.













Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) imetoa utaratibu rasmi wa uombaji wa vibali vya kusimika mabango kando ya barabara, ikiwa ni hatua ya kukabiliana na matapeli wanaojifanya watumishi wa taasisi hiyo na kuwahadaa wafanyabiashara.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, wananchi wanaotaka kuweka mabango wanapaswa kuwasilisha maombi yao kwa njia ya barua rasmi kwa wakala, wakieleza kwa kina ujumbe wa tangazo, ukubwa wa bango (kwa mita za mraba), pamoja na namba ya simu ya mawasiliano.

Hatua inayofuata itahusisha ukaguzi wa eneo lililopendekezwa kufungwa bango, ambapo maafisa wa TANROADS watathibitisha kama eneo hilo linakidhi vigezo vinavyotakiwa, Endapo mwombaji atakidhi vigezo, atapewa barua ya malipo yenye namba ya kumbukumbu (control number) kwa ajili ya kukamilisha malipo husika.

Baada ya kufanya malipo, mwombaji atapatiwa kibali rasmi cha kusimika bango, ambacho kitakuwa halali kwa kipindi cha mwaka mmoja, TANROADS imefafanua kuwa baada ya muda huo kuisha, mmiliki wa bango atalazimika kulipia upya ili kuhuisha kibali chake na kuendelea kutumia eneo hilo.

Wakala huo umewataka wananchi kuwa makini na watu wanaojitambulisha kama watumishi wake bila uthibitisho rasmi, na kusisitiza kuwa taratibu zote za maombi na malipo zinapaswa kufanywa kupitia njia rasmi zilizoainishwa.





Wataalamu kutoka Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC) wamehitimisha mafunzo maalum ya ulinzi na usalama dhidi ya mionzi kwa wafanyakazi wa Maweni Limestone Company. Mafunzo haya, yaliyofunguliwa na Meneja wa Idara ya Ubora wa kampuni hiyo, yalilenga kuwajengea uwezo wafanyakazi wanaoshughulika moja kwa moja na vifaa vya X-Ray Fluorescence (XRF) na nuclear gauges.

Kwa muda wa siku kadhaa, washiriki walipata nafasi ya kujifunza kwa kina kuhusu utambulisho wa mionzi ayonishi, kiasi cha mionzi na vipimo, matumizi ya mionzi, athari zake kiafya, kanuni za ulinzi, mfumo wa kisheria wa Tanzania, majukumu ya Afisa Usalama wa Mionzi (RSO), pamoja na usalama wa nyuklia na udhibiti wa usafirishaji haramu.

Katika hotuba ya kufunga mafunzo, wataalamu wa TAEC walisisitiza umuhimu wa kuimarisha utamaduni wa usalama kazini. “Tunataka kuona kila mfanyakazi akibeba jukumu la kulinda afya yake, wenzake na jamii kwa ujumla. Usalama wa mionzi si jambo la hiari, ni wajibu wa kitaifa,” alieleza Ndugu Mungubariki Nyaki, mkufunzi na msimamizi wa Ofisi ya TAEC Jijini Tanga.

Washiriki walionekana wenye shauku na ari ya kupeleka maarifa mapya kazini. Baadhi walikiri kuwa mafunzo haya yamewapa ujasiri wa kushughulika na vifaa vya mionzi kwa umakini zaidi, huku wengine wakisisitiza umuhimu wa kushirikiana na TAEC ili kuhakikisha viwango vya kitaifa na kimataifa vinazingatiwa.

Mafunzo haya pia yaligusia hatua za dharura endapo ajali za mionzi zitatokea, jambo lililowapa washiriki uelewa wa namna ya kukabiliana na changamoto kwa utulivu na ufanisi.

Kwa ujumla, kufungwa kwa mafunzo haya kumeacha taswira ya matumaini na uwajibikaji. Kampuni ya Maweni Limestone imeonyesha dhamira ya dhati ya kulinda wafanyakazi wake na jamii kwa kuhakikisha teknolojia za kisasa zinatumika kwa usalama na kwa manufaa ya Taifa.





Pamela Mollel Arusha 

MAWAKALA WA BIMA wametakiwa kuzingatia  uadilifu, pamoja na kujenga mahusiano imara na wateja, pamoja na kuendelea kujifunza ili kuendana na mabadiliko ya soko.

Hayo yamesemwa  jijini Arusha na  Meneja wa Bima kanda ya kaskazini (TIRA) Dokta  Emmanuel Lupilya wakati akizungumza kwenye kikao maalumu kilichowakutanisha mawakala wa bima kutoka jijini Arusha .

Dokta Lupilya amesema lengo la kikao hicho ni kujadili na kuweza kuboresha maswala mbalimbali ya bima pamoja na kusikiliza changamoto zinazowakabili na kuzipatia ufumbuzi wa haraka.

Dokta Lupilya amesema kuwa,Wakala wa bima wametambuliwa kwa mchango wao mkubwa katika kulinda maisha na mali za Watanzania .

Dokta Lupilya amesema kuwa,kusanyiko hilo limewaleta kutambua mchango mkubwa hasa kwa mawakala wanaofanya kwa ajili ya  nchi yetu  .

"Ni dhahiri kuwa wanaendesha biashara hizi kwa kuzingatia weledi kwa  kuthamini utu wa wananchi pamoja na udhubutu wao katika kuhakikisha wanalinda ndoto za watanzania ."amesema .

Ameongeza  kuwa, mafanikio  yao wanayofanya yasihesabiwe tu katika mikataba wanayoandika bali ihesabiwe katika watu wangapi wamewahubiria habari za bima watu wangapi wamewasaidia katika maswala yao pamoja na familia walizosaidia katika kuingia kwenye mfumo mzima wa bima .

"Kwa kufanya hivyo watakuwa wamehesabiwe ile thamani yao kwa kuelimisha jamii na imani waliyoonyesha kwa jamii kuwa bima sasa sio kitu cha anasa bali  ni kitu cha muhimu na kila mwananchi lazima awe nacho ."amesema Dokta Lupilya. 

"Swala la kutoa huduma z bima sio swala dogo ni swala zito na ni swala ambalo linahitaji weledi zaidi na mawakala hawa wamekuwa mfano wa kuigwa kwani wamekuwa lango la kuwezesha uelewa wa maswala la bima kwa  jamii."amesema .

"Kilio changu mimi ni kuhakikisha kuwa kukua kwa sekta ya bima kuna mchangao mkubwa sana wa mawakala  kuwezesha sekta kukua na mawakal hao wanafanya kazi kubwa ."amesema  Dokta Lupilya. 

 Amesema kuwa lengo ni kuhakikisha mawakala wanakuwa na wao kama  mamlaka ni kuhakikisha wanawawekea mazingira rafiki ambayo yatawawezesha kufanya kazi kwa uadilifu mkubwa .

Aidha amewataka pia mawakala kufanyiwa mafunzo mara kwa mara katika maswala ya fedha ili wajue namna ya kutunza kile wanachokipata .

Aidha ametoa kwa makampuni kuonyesha mfano kwa maana ya kupeleka mafunzo ya maswala ya mahesabu ili wajue namna ya kuweza kukua na kuweza kujifunza teknolojia mpya kwani kuna wakati wataanza kuuza bidhaa zao kupitia teknolojia kwan8 teknolojia inauza zaidi .

"Tuwafundishe hawa namna ya kutumia teknolojia kwenye biashra ya bima na kwa kufanya hivyo tutafanikiwa kwa kiwango kikubwa sana ."amesema Dokta Lupilya. 

Nao Baadhi ya mawakala wakizungumza kwenye kikamo hicho , wamesema kuwa ,malalamiko makubwa wanayolalamikia.ni swala la mzigo mkubwa ambao mawakala wanayabeba jambo ambalo mawakala wengi wanashindwa kuendesha hiyo biashara kutokana na changamoto hizo kwani soko limekuwa na ushindani mkubwa na gharama za uendeshaji zimekuwa kubwa kwani mabenki yameingia ambapo ameomba mamlaka hiyo iangalie namna ya kuwabeba mawakala na mawakala ndo wenye biashara ya moja kwa moja .

"Tunachoomba mhakikishe mnawabeba hawa mawakala kwani mzigo ni mkubwa sana na hawawezi na mjitahidi  kuwawezesha mawakala na muwape  motisha pia ."amesema .







KILIO cha muda mrefu cha wananchi wa Kata ya Njiapanda, wilayani Moshi, kuhusu ubovu wa barabara uliosababishwa na mvua, kimeanza kupatiwa ufumbuzi baada ya Diwani wa kata hiyo kwa kushirikiana na wananchi kumwaga vifusi ili kurejesha mawasiliano ya barabara.

Hatua hiyo imewaibua Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) wakidai kuendelea kutafuta fedha kwa matengenezo ya kudumu.

 Wananchi wa maeneo ya Njiapanda Mashariki, Magharibi, Samunge,  na vitongoji jirani wamekuwa wakikumbwa na changamoto kubwa ya mawasiliano  kutokana na barabara kuharibika vibaya kufuatia mafuriko ya mvua, hali inayosababisha mkwamo wa shughuli za kijamii na kiuchumi.

Akizungumzia hali hiyo, Mwenyekiti wa wachimbaji katika eneo la mgodi wa Samunge, Samson Laizer, alisema barabara ya kuelekea migodini imeathirika kwa kiasi kikubwa na kusababisha shughuli za uchimbaji kusuasua.

Aliongeza kuwa hali hiyo imekuwa ikiathiri pia wanafunzi kushindwa kwenda shule pamoja na wafanyabiashara kushindwa kusafirisha bidhaa kama kokoto, mawe, udongo na mchanga kutoka migodini.

Kwa upande wake, Faustin Abel mkazi wa Njiapanda Mashariki alisema kipindi cha mvua watoto hushindwa kwenda shule na hata wananchi wengine kushindwa kwenda ibada kutokana na ubovu wa barabara.

“Kwa kushirikiana na diwani wetu, tumeanza kuchukua hatua za dharura kwa kumwaga vifusi na kuchimba mitaro kwa nguvu za wananchi ili kurahisisha upitishaji wa magari na watu, kwa muda wakati tukisubiri matengenezo ya kudumu,” alisema.

Mwenyekiti wa Kitongoji cha Njiapanda Mashariki, Sadick Kanyika, alisema kitongoji hicho chenye wakazi zaidi ya 7,500 kimeathirika kwa kiasi kikubwa na mafuriko, huku barabara muhimu ikiwemo ya ofisi ya mtendaji ikiharibika vibaya.

Naye Donsia Andrea mkazi wa Otomoro alisema hali hiyo imekuwa hatari zaidi kwa kina mama wajawazito na wagonjwa, akieleza kuwa baadhi yao hulazimika kujifungulia njiani kutokana na kushindwa kufikishwa hospitalini kwa wakati.

Kutokana na hali hiyo, Diwani wa Kata ya Njiapanda ambaye pia ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Moshi, John Meela, alisema wameanza hatua za dharura za kurekebisha barabara hizo kwa kushirikiana na wananchi.

“Tumeanza kuboresha barabara zilizoathiriwa na mvua kwa kumwaga vifusi kwenye maeneo korofi, zikiwemo barabara ya Samunge, Ofisi ya Kata–Otomoro, Kilototoni–Zahanati na nyinginezo. Barabara ya Samunge–Migodini ni muhimu kiuchumi kwa kuwa inahudumia shughuli za uchimbaji, hivyo inahitaji pia uwekaji wa makalvati ili kudhibiti maji ya mvua,” alisema Meela.

Alieleza kuwa tayari wamewasiliana na TARURA ambao wamefanya ukaguzi wa barabara hizo na kuahidi kutafuta fedha za dharura kwa ajili ya matengenezo ya haraka.

Kwa upande wake, Meneja wa TARURA Wilaya ya Moshi, Godfrey Mbena, alisema mtandao wa barabara unaohudumiwa na wakala huo katika Halmashauri ya Moshi, una urefu wa kilometa 827.71, ambapo kilometa 41.65 ni za lami, kilometa 337.16 ni za changarawe na kilometa 448.9 ni za udongo.

Alisema mvua zimeathiri kwa kiasi kikubwa barabara nyingi vijijini, ikiwemo katika kata ya Njiapanda huku changamoto kubwa ikiwa ni upungufu wa fedha kulinganisha na mahitaji halisi.

“Tumefanya tathmini ya barabara zilizoathirika na kuziwasilisha kwa ajili ya kupata fedha za matengenezo. Kwa sasa tumeomba zaidi ya shilingi bilioni 3 kwa ajili ya Wilaya ya  Moshi na tunaamini serikali itatoa fedha hizo ili kuanza matengenezo,” alisema.







KAMPUNI ya Taifa Gas imetangaza kuwa haitapandisha bei ya gesi ya majumbani (LPG) licha ya kupanda kwa bei ya bidhaa hiyo kwa takribani asilimia 43 katika soko la kimataifa, hatua inayolenga kulinda watumiaji dhidi ya athari za mabadiliko ya kiuchumi duniani.

Taarifa hiyo iliyotolewa leo Aprili 3, 2026 jijini Dar es Salaam imeeleza kuwa ongezeko hilo la bei duniani limechangiwa na kupanda kwa gharama katika minyororo ya ugavi na usambazaji wa gesi ya kupikia katika wiki za hivi karibuni.

Akizungumza kupitia taarifa hiyo, Meneja Mkuu wa kampuni hiyo, Devis Deogratius, amesema licha ya changamoto hizo, kampuni imeamua kubeba gharama hizo ili kuhakikisha wateja wanaendelea kupata huduma kwa bei nafuu.

“Katika mazingira haya ya sasa, tunayo dhamira ya dhati ya kuwasaidia wateja wetu kwa kubeba athari za ongezeko la gharama ya nishati ya kupikia kwa kutokuongeza bei huku tukihakikisha upatikanaji endelevu wa gesi safi na ya kuaminika,” amesema Deogratius.

Amesisitiza kuwa uamuzi huo unalenga kusaidia shughuli za kiuchumi, hasa kwa kaya na biashara ndogo ndogo zinazotegemea gesi ya kupikia kama chanzo kikuu cha nishati.

Deogratius amebainisha kuwa Taifa Gas inaelewa umuhimu wa nishati hiyo kwa Watanzania wengi, hivyo itaendelea kuhakikisha inapatikana kwa bei nafuu bila kuathiri usambazaji wake.

Aidha, kampuni hiyo imehakikishia umma kuwa itaendelea kusambaza gesi yake kwa uhakika kupitia mtandao wake wa maghala 25 yaliyosambaa nchini, hatua inayolenga kufikia wateja wa mijini na vijijini.

"Uwekezaji uliofanywa katika miundombinu ya usambazaji unaiwezesha kampuni hii kuhudumia maeneo mbalimbali ya nchi kwa ufanisi zaidi na kuendelea kuunga mkono ajenda ya kitaifa na kimataifa ya nishati safi.

Aidha amesema wataendelea kufuatilia mwenendo wa soko la kimataifa na kufanya maamuzi yatakayolinda maslahi ya wateja huku ikidumisha ubora wa huduma zake.
Wito umetolewa kwa wawekezaji na wazalishaji nchini kutumia huduma za Shirika la Viwango Tanzania (TBS), hususan katika sekta ya vipimo (metrolojia), kutokana na kutambulika kwake kimataifa.

Akizungumza na wanahabari Aprili, 2, 2026 jijini Dar-es-Salaam, Afisa Mkuu wa Metrolojia Joseph Kadenge kutoka Shirika la Viwango Tanzania (TBS) amesema kuwa Metrolojia (Sayansi ya Vipimo) ni Moja ya Misingi minne ya Ubora inayoangalia ubora wa vipimo katika mashine zinazotumika katika uzalishaji.

Amesema ubora wa bidhaa unaanzia kwenye mashine zinazozalishia, kama mashine hazina vipimo sahihi basi hata ubora wa bidhaa uko mashakani.

Kadenge ameongeza kuwa TBS ina Maabara ya Taifa (National Metrology Laboratory) ya Vipimo inayotambulika kimataifa kupitia Shirika la Vipimo Duniani (BIPM), huku uwezo wake wa upimaji ukiwa umeorodheshwa katika kanzidata ya kimataifa.

Aidha, maabara hizo zimepata ithibati ya umahiri kutoka taasisi ya kuangalia umahili ya nchi za SADC inayoitwa SADCAS, hatua inayothibitisha ubora wa huduma zake na kuwahakikishia wawekezaji kuwa huduma za vipimo zinapatikana kwa viwango vinavyokubalika kimataifa.

Kupitia umahiri huo, Kadenge ametoa wito kwa wawekezaji na wazalishaji kutokuwa na hofu ya kuwekeza Tanzania kwani upatikanaji wa huduma ya Ugezi (Calibration) zinapatikana kwa urahisi.





Na Karama Kenyunko Michuzi Tv

WAZIRI wa Afya, Mohamed Mchengerwa, amesema Serikali inaendelea kuchukua hatua madhubuti za kuboresha upatikanaji wa dawa na bidhaa za afya katika vituo vyote vya kutolea huduma nchini, huku akisisitiza umuhimu wa kuimarisha mifumo ya ugavi ili kuhakikisha dawa zinapatikana kwa wakati na kwa ubora unaokidhi viwango.

Amesema hayo Aprili 2, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa kikao kazi na wadau wa sekta ya afya kilichofanyika katika Bohari ya Dawa (MSD), Keko, ambapo alibainisha kuwa uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali umeendelea kuimarisha hali ya upatikanaji wa dawa na kufikia viwango vinavyoridhisha.

“Serikali imeendelea kuboresha mifumo ya usimamizi na ugavi ili kuhakikisha dawa zinafika kwa wakati katika maeneo yote ya nchi. Maboresho haya yanachangia kupunguza changamoto ya upungufu wa dawa katika vituo vya afya,” amesema Mchengerwa.

Aidha, amesema Serikali imeelekeza juhudi katika kuhakikisha kunakuwepo uwiano sahihi kati ya mahitaji halisi na upatikanaji wa dawa, hatua inayosaidia kuongeza ufanisi na matumizi bora ya rasilimali zilizopo.

Katika kikao hicho, Mchengerwa alisisitiza pia umuhimu wa Bohari ya Dawa (MSD) kuendelea kuimarisha mifumo ya usimamizi, manunuzi na usambazaji wa dawa ili kuepuka upungufu katika vituo vya kutolea huduma.

Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Serikali, Grace Magembe, amesema Serikali itaendelea kusimamia matumizi sahihi ya dawa pamoja na kuhakikisha upatikanaji wake katika ngazi zote za huduma za afya nchini.

Dkt. Magembe alisisitiza kuwa dawa si bidhaa ya kawaida bali ni kemikali yenye uwezo wa kutibu au kusababisha madhara iwapo haitatumika kwa usahihi, hivyo usambazaji wake lazima uzingatie uwepo wa wataalamu wenye ujuzi pamoja na miundombinu ya kumhudumia mgonjwa endapo atapata madhara.

Akijibu hoja za wananchi, alisema Serikali inatambua changamoto zilizopo, ikiwemo upatikanaji wa baadhi ya dawa katika zahanati na vituo vya afya, na kwamba hatua zinaendelea kuchukuliwa ili kuboresha hali hiyo.

Kuhusu upatikanaji wa dawa katika ngazi mbalimbali, alisema upangaji wake unazingatia tafiti za kisayansi na Orodha ya Dawa Muhimu (Essential Drug List), ambapo kila ngazi hupangiwa dawa kulingana na aina ya huduma na uwezo wa kituo husika.

Akizungumzia suala la dawa kuisha muda wake (expiries), Dkt. Magembe alisema hali hiyo ni ya kawaida duniani kote kutokana na muda wa matumizi wa dawa na mabadiliko ya kisayansi, na kusisitiza kuwa Serikali haiwezi kuruhusu matumizi ya dawa zisizo na ufanisi.

Alibainisha kuwa kiwango cha dawa zinazoisha muda wake nchini ni asilimia 1.2, chini ya kiwango kinachokubalika kimataifa cha asilimia tano, jambo linaloonesha usimamizi mzuri.

Aidha, alisema Serikali imeanza kushusha huduma za magonjwa adimu kama sickle cell hadi ngazi ya hospitali za wilaya na kuingiza dawa zake katika mfumo wa ununuzi ili kupunguza gharama kwa wananchi.

Dkt. Magembe pia aligusia matumizi ya majina ya dawa (brand names badala ya generic names), akisema Serikali itatoa maelekezo kurekebisha hali hiyo ili kuongeza ufanisi katika upatikanaji wa dawa.

Aliongeza kuwa Serikali imeongeza bajeti ya dawa kutoka takribani shilingi bilioni 30 hadi kufikia bilioni 398 mwaka 2025, hatua iliyosaidia kuongeza upatikanaji wa dawa hadi asilimia 88 kwa sasa.

“Tutajipanga zaidi kutoa elimu kwa wananchi waelewe sayansi ya dawa na matumizi yake, kwa sababu dawa si chakula; ni sumu isipotumika vizuri,” amesema Dkt. Magembe.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Seif Shekalaghe, amesema zaidi ya asilimia 60 ya wagonjwa wanaokwenda hospitali hupatiwa dawa, huku wengine wakipewa ushauri wa mabadiliko ya mtindo wa maisha ikiwemo mazoezi.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Bohari ya Dawa (MSD), Mavere Tukai, amesema taasisi hiyo imeendelea kuboresha utendaji wake kwa kuimarisha mifumo ya kidijitali, kuongeza ufanisi katika manunuzi na kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi.

Ameeleza kuwa ununuzi wa bidhaa za afya kutoka kwa wazalishaji wa ndani umeongezeka kutoka shilingi bilioni 15.9 mwaka 2021/2022 hadi bilioni 98 mwaka 2024/2025, huku lengo la mwaka huu likiwa kufikia kati ya bilioni 120 hadi 130.

Aidha, amesema utegemezi kwa wasambazaji wa nje umepungua kutoka asilimia 82 hadi asilimia 38, wakati ununuzi kutoka kwa wazalishaji wa ndani umeongezeka hadi asilimia 75.

Alibainisha kuwa hatua hizo zimewezesha hata dawa ambazo awali zilikuwa ngumu kupatikana, ikiwemo za saratani, kupatikana kwa urahisi zaidi na kwa gharama nafuu.

Kikao hicho ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuendelea kuimarisha sekta ya afya na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora nchini.

Waziri wa Afya Mohamed Mchengerwa akizungumza na Wananchi mubashara kupitia mfumo ongea na Waziri kupitia namba ya 199, leo Aprili 2, 2026, wakati wa kikao kazi na wadau wa Afya kilichofanyika Bohari ya Dawa, jijini Dar es Salaam









Top News