Na Pamela Mollel,Arusha 

Jitihada za kuhakikisha Watanzania wengi zaidi wanapata huduma za nishati safi ya kupikia zimepewa msukumo mpya baada ya wadau kutoka sekta ya umma, binafsi na mashirika ya maendeleo kukutana jijini Arusha kujadili mikakati ya kuharakisha upatikanaji wa nishati hiyo nchini. Mkutano huo umejadili fursa, changamoto na mbinu za kuongeza matumizi ya teknolojia za kupikia ambazo ni salama kwa afya na mazingira.

Akifungua mkutano huo, Naibu Waziri wa Nishati, Salome Makamba, alisema Tanzania imepata mafanikio makubwa katika utekelezaji wa ajenda ya nishati safi ya kupikia, ambapo kiwango cha matumizi kimeongezeka kutoka asilimia 6.9 mwaka 2021 hadi asilimia 28.6 mwaka 2025. Alisema ongezeko hilo linaonesha namna juhudi za Serikali na ushirikiano wa wadau mbalimbali zinavyoendelea kuleta matokeo chanya katika kuboresha maisha ya wananchi.

Makamba alibainisha kuwa Serikali imeweka lengo la kuhakikisha asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034 kupitia utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia wa mwaka 2024–2034. Alisema mkakati huo umejikita katika kuongeza upatikanaji wa teknolojia nafuu za kupikia, kuimarisha ushiriki wa sekta binafsi na kuhamasisha wananchi kubadili matumizi ya nishati za jadi zinazochangia uharibifu wa mazingira.

Alieleza kuwa mafanikio yaliyofikiwa hadi sasa yamechangiwa na utekelezaji wa miradi mbalimbali ikiwemo usambazaji wa mitungi 452,445 ya gesi ya LPG, majiko banifu zaidi ya 200,000 pamoja na mradi wa CookFund unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya kupitia UNCDF. Miradi hiyo imewezesha mamia ya maelfu ya wananchi katika mikoa mbalimbali kupata huduma za nishati safi na salama ya kupikia.

Katika mkutano huo, Balozi wa Umoja wa Ulaya nchini Tanzania, Christine Grau, alitangaza kuwa EU imetenga euro milioni 30, sawa na zaidi ya shilingi bilioni 92, kwa ajili ya kusaidia upanuzi wa matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini. Alisema uwekezaji huo unalenga kuimarisha masoko ya nishati endelevu, kuvutia uwekezaji wa sekta binafsi na kuongeza upatikanaji wa huduma kwa wananchi wa maeneo ya mijini na vijijini.

Grau alisema ufadhili huo ni sehemu ya mkakati wa Global Gateway unaolenga kuharakisha maendeleo endelevu kupitia uwekezaji katika sekta muhimu za kiuchumi. Alisisitiza kuwa matumizi ya nishati safi ya kupikia yana mchango mkubwa katika kulinda mazingira, kupunguza ukataji wa miti na kuboresha afya za wanawake na watoto ambao mara nyingi huathiriwa na moshi unaotokana na matumizi ya nishati za jadi.

Kwa mujibu wa wadau walioshiriki mkutano huo, ushirikiano kati ya Serikali, washirika wa maendeleo na sekta binafsi utaendelea kuwa nguzo muhimu katika kufanikisha ajenda ya nishati safi ya kupikia nchini. Walisema hatua zinazochukuliwa kwa sasa zinaipa Tanzania nafasi nzuri ya kufikia malengo yake ya mwaka 2034 huku zikichangia ustawi wa wananchi, uhifadhi wa mazingira na maendeleo ya uchumi wa taifa kwa ujumla.






Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, akiwa katika picha ya pamoja na Bw. Massad Boulos, mwanadiplomasia na Mshauri Mwandamizi wa Rais Donald Trump kuhusu masuala ya Afrika, nchi za Kiarabu na Mashariki ya Kati, baada ya kufanya mazungumzo pembezoni mwa Mkutano wa Oslo Forum unaofanyika Oslo, Norway.


Mkutano huo, unaofanyika kuanzia tarehe 10 hadi 12 Juni, 2026, umewakutanisha viongozi, wanadiplomasia waandamizi na wadau wa masuala ya amani, diplomasia na usuluhishi kutoka nchi mbalimbali zenye ushawishi duniani.

Kamishna wa Uhifadhi TANAPA, CPA Musa Nassoro Kuji amekabidhi kwa Bodi ya Wadhamini ya TANAPA Tuzo ya Mafanikio katika Utoaji wa Huduma bora Mwaka 2026 (Quality Achievement Award 2026) pamoja na Cheti cha Ushindi wa Pili (First Runner-Up) katika Tuzo za Ubora wa Taifa 2025/2026 kwenye kikao cha bodi hiyo kinachoendelea leo Juni 11, 2026 jijini Dar es salaam.

Tuzo ya “Quality Achievement Award 2026” ilitolewa tarehe 31 Mei 2026 jijini Brussels, Ubelgiji na Taasisi ya “European Society for Quality Research (ESQR)” huku Cheti cha Ushindi katika Tuzo za Ubora wa Taifa 2025/2026 kilitolewa na Shirika la Viwango Tanzania kwa kutambua taasisi zinazofanya vizuri katika utoaji wa huduma na kuzingatia viwango vya ubora, kilitolewa juni 05, 2026 jijini Dar es salaam.

Bodi ya Wadhamini TANAPA inayoongozwa na Mwenyekiti wake  Jenerali George Waitara, Mkuu wa Majeshi Mstaafu, imepokea tuzo hizo na kuipongeza Menejimenti ya Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania, Maafisa na Askari Uhifadhi kwa kuendelea kutambulika kimataifa na kitaifa katika kusimamia utekelezaji wa majukumu ya TANAPA ya uhifadhi na maendeleo ya utalii nchini. 

Vilevile, Bodi ya Wadhamini imetoa wito kwa watumishi wote wa Shirika kuhakikisha kuwa kila mmoja anatimiza wajibu wake kikamilifu ili kuendelea kufanikisha malengo ya Shirika na Taifa kwa ujumla pamoja na kupata tuzo nyingi zaidi.










London, Juni 10, 2026: Airtel Africa Plc (“Airtel Africa”), 
KAMPUNI inayoongoza katika utoaji wa huduma za mawasiliano na huduma za kifedha kwa njia ya simu katika nchi 14 barani Afrika ikiwemo Tanzania, imechapisha Ripoti yake ya Maendeleo ya 2026, inayobainisha mafanikio yaliyopatikana katika kupanua huduma za mawasiliano, kuimarisha ujumuishi wa kifedha na kuchochea maendeleo endelevu katika jamii inazohudumia kwa kipindi cha mwaka wa fedha 2025/26.

Ripoti hiyo inaonesha jinsi uwekezaji wa Airtel Africa katika miundombinu ya kidijitali, huduma za kifedha kupitia simu za mkononi, pamoja na ushirikiano wa kimkakati, ulivyoendelea kubadilisha maisha ya watu na kufungua fursa za kiuchumi na kijamii kwa jamii ambazo bado hazijafikiwa kikamilifu na huduma hizo, hususan katika nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara.

Aidha, ripoti hiyo inaeleza hatua mbalimbali zinazoendelea kuchukuliwa na Airtel Africa katika matumizi ya nishati mbadala, pamoja na mbinu zake za kuendesha biashara kwa kuzingatia uwajibikaji, uhifadhi wa mazingira na uwazi katika utoaji wa taarifa za maendeleo kwa wadau wake.

Akizungumzia ripoti hiyo, Mtendaji Mkuu wa Airtel Africa, Sunil Taldar, alisema:

"Barani Afrika, upatikanaji wa mawasiliano, huduma za kifedha na elimu ya kidijitali unazidi kuwa muhimu katika kufungua fursa za kiuchumi. Airtel Africa inaendelea kupanua huduma hizi kwa mamilioni ya watu, hususan katika maeneo ya vijijini na yale ambayo bado hayajafikiwa kikamilifu."

“Katika mwaka huu, tumeendelea kupanua huduma za mtandao, kuongeza matumizi ya simu janja na kuimarisha huduma za Airtel Money, sambamba na kuendeleza ushirikiano wa kimkakati unaochangia mafanikio ya shughuli zetu. Maendeleo haya yameendelea kuwa sehemu muhimu ya mkakati wetu wa kukuza biashara na kutoa huduma bora kwa wateja. Aidha, kwa kuboresha matumizi ya nishati na kupunguza utegemezi wa dizeli, tunaimarisha ufanisi na ustahimilivu wa shughuli zetu, huku tukichangia ukuaji endelevu wa biashara na jamii.”

Vigezo muhimu vya Mazingira, Jamii na Utawala Bora (ESG) kwa Mwaka 2025/26

1. Kupanua Mawasiliano na Kupunguza Pengo la Kidijitali

● Watu wanaofikiwa na mtandao wa simu umefikia asilimia 81.9, kutoka asilimia 81.2 mwaka 2024/25.

● Upatikanaji wa huduma za mtandao katika maeneo ya vijijini umeongezeka hadi asilimia 73.1, kutoka asilimia 72.2 mwaka uliotangulia.

● Idadi ya wateja wanaotumia huduma za data umeongezeka hadi asilimia 45.9, kutoka asilimia 44.2.

● Matumizi ya simu janja yaliongezeka hadi asilimia 49.5, kutoka asilimia 44.8, hatua inayowezesha watu wengi zaidi kupata huduma za mtandao na majukwaa ya kidijitali.

● Thamani ya miamala iliyofanyika kupitia programu ya My Airtel imefikia dola za Marekani bilioni 8.3, ikiwa ni ongezeko la asilimia 80 ikilinganishwa na mwaka uliopita, huku watumiaji hai wa kila mwezi wakifikia milioni 10.5.

2. Kuimarisha Ujumuishaji wa Kifedha na Ushiriki wa Kiuchumi

● Idadi ya wateja wa Airtel Money imeongezeka na kufikia zaidi ya milioni 54, kutoka milioni 44.6 mwaka 2024/25.

● Asilimia 44.1 ya wateja wa Airtel Money ni wanawake.

● Thamani ya miamala iliyochakatwa kupitia Airtel Money ni takribani dola za Marekani bilioni 196, kutoka dola bilioni 136 mwaka uliopita.

3. Kusaidia Elimu, Ujuzi na Fursa za Ajira

● Mtandao wa mawakala wa Airtel Money uliongezeka na kufikia mawakala milioni 2.4, kutoka milioni 1.7 mwaka 2024/25, hatua inayochangia ujasiriamali, ajira na upatikanaji wa huduma za kifedha.

● Uwiano wa wanawake katika nguvu kazi ya Airtel Africa uliongezeka hadi asilimia 29.9, kutoka asilimia 29.2 mwaka uliopita.

● Kufikia Machi 31, 2026, jumla ya shule 3,043 zilikuwa zimeunganishwa na huduma za intaneti bila malipo kupitia ushirikiano kati ya Airtel Africa Foundation na UNICEF, kutoka shule 2,176 mwaka 2024/25.

4. Kupunguza Athari za Mazingira Zinazotokana na Shughuli za Kampuni

● Zaidi ya maeneo 950 ya miundombinu ya kampuni yalibadilishwa kutoka matumizi ya nishati isiyounganishwa na gridi ya taifa kwenda kwenye umeme wa gridi ya taifa, kutoka maeneo 500 mwaka uliopita.

● Matumizi ya dizeli yalipunguzwa kwa lita milioni 9.1 katika kipindi cha mwaka mmoja.

● Asilimia 94 ya taka zote zilizozalishwa zilirejelewa (recycled), ikilinganishwa na asilimia 93 mwaka 2024/25.

Ripoti ya Maendeleo ya 2026 imeandaliwa kwa kuzingatia viwango vya kimataifa vya Global Reporting Initiative (GRI) pamoja na miongozo ya sekta ya mawasiliano ya simu ya GSMA.
Kuhusu Airtel Africa

Airtel Africa ni mtoa huduma wa mawasiliano na huduma za fedha kwa njia ya simu anayehudumia zaidi ya wateja milioni 183.5 katika nchi 14 za Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara. Kampuni inalenga kuendeleza ujumuishi wa kidijitali na kifedha kwa kuwafungulia wananchi fursa za maendeleo na kuboresha maisha yao kupitia huduma za mawasiliano na teknolojia.

Mdhibiti Ubora Mkuu wa NACTVET Nicholaus Moshi akizungumza na Waandishi wa habari kuhusiana na Shindano la Ubunifu wa Ushonaji wa Mavazi kwa Kanda ya Dar es Salaam lililofanyika Chuo cha Anna Academy.Mkurugenzi wa Chuo cha Anna Academy Anna Lunguya akizungumza kuhusiana mashindano hayo katika ubunifu wakiwa ndio watarajiwa wa kuiwakilisha nchi kudunia katika mashindano baada ya kufanyika mchujo wa kitaifa.

Washiriki Tisa wakijiandaa katika shindano la ubunifu wa Ushonaji wa  mavazi.

Picha katika Makundi mbalimbali wakati wa maandalizi ya Shindano la Ubunifu wa Ushonaji Mavazi lililofanyika katika Chuo cha Anna Academy.

Na Chalila Kibuda, Michuzi TV
NCHI  ya Tanzania kushiriki mashindano ya ubunifu na ubobezi wa katika Fani Tisa kwa kushirikisha wanafunzi wa Vyuo vya Ufundi Stadi ambapo washindi wataopatikana katika Kanda wataingia ngazi Kitaifa watachunjwa kujiandaa kuwakilisha nchi kidunia.

Mkurugenzi wa Udhibiti Ubora wa NACTVET Joffrey Oleke amesema mashindano yalianza katika ngazi ya vyuo ambao washindi wanaingia katika mashindano ya kikanda.

Mashindano katika Fani ya ubunifu wa Ushonaji wa Mavazi Kanda ya Dar es Salaam yamefanyika katika Chuo cha Anna Academy kwa washiriki Tisa katika fani hiyo ambapo Katika mchujo watabaki wa tano ambao wataingia katika mashindano ya Kitaifa yatayofanyika mkoani Tanga Agasti Mwaka huu.

Akizungumza kwenye Mashindano Ubunifu wa Ushonaji wa Mavazi Mdhibiti Ubora Mkuu wa NACTVET Kanda ya Mashariki, Nicholaus Moshi, amesema mashindano hayo ni jukwaa muhimu la kuibua vipaji, kukuza ubunifu na kuandaa vijana watakaoiwakilisha Tanzania katika mashindano ya ngazi za kikanda na kimataifa.

Washiriki Tisa wanatoka maeneo mbalimbali ambao wanapimwa uwezo wao katika ubunifu, ukataji na ushonaji wa mavazi kwa kutumia viwango vya kimataifa.

Amesema washiriki hao wanatarajiwa kuchujwa ili kupata washindi watakaowakilisha Tanzania katika hatua zinazofuata za mashindano ya ujuzi ngazi ya kikanda na kimataifa.

“Mashindano haya yanalenga kupima uwezo wa vijana wetu katika ubunifu, ushonaji na matumizi ya teknolojia ya kisasa katika sekta ya mavazi. Tunafurahi kuona vijana wameandaliwa vizuri kisaikolojia, kitaaluma na kwa vitendo ili kuonyesha uwezo wao,” amesema Moshi.

Ameongeza kuwa vifaa vinavyotumika katika mashindano hayo ni vya kisasa na vinavyotumika katika tasnia ya ubunifu na ushonaji duniani kote, jambo linalowawezesha washiriki kupata uzoefu unaokidhi viwango vya kimataifa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Ana Collection Academy, Anna Lunguya, amesema taasisi hiyo inajivunia kuwa mwenyeji wa mashindano hayo ambayo yana mchango mkubwa katika kukuza sekta ya ubunifu na ushonaji nchini.

Amesema sekta ya ubunifu na ushonaji imekuwa chanzo muhimu cha ajira na biashara kwa vijana wengi, hivyo mashindano hayo yatasaidia kuibua vipaji vipya na kupata wabunifu watakaoweza kuiwakilisha Tanzania katika ngazi mbalimbali za Afrika na duniani.

Na Hassan Kimweri, WAF – Tabora.

Jumla ya macho 996 yamefanyiwa uchunguzi kwa wagonjwa 823 wanaotarajiwa kufanyiwa upasuaji wa mtoto wa jicho katika kambi maalum ya madaktari bigwa iliyowekwa na Serikali kwa kushirikiana na Taasisi ya 'Helen Keller International' na wadau wengine wa sekta ya afya.  

Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Igunga Mhe. Elizabeth Rwegasila amesema hayo leo wakati wa ufunguzi wa kambi ya madaktari bingwa wa macho iliyowekwa katika Hospitali ya Wilaya ya Igunga mkoani Tabora ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuboresha afya ya macho na kuondoa tatizo la upofu kwa wananchi. 

"Idadi hii inaonesha ukubwa wa mahitaji ya huduma za macho kwa wananchi wa eneo hili, wanaonufaika na huduma hiyo wanapatiwa huduma mbalimbali muhimu ikiwemo usafiri kutoka majumbani mwao, malazi, chakula pamoja na huduma za matibabu kabla na baada ya upasuaji," amesema Mhe. Rwegasila

Aidha, amelishukuru Shirika la Helen Keller International kwa kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuboresha huduma za afya ya macho, akieleza kuwa mbali na kutoa huduma za matibabu, shirika hilo limechangia kuwajengea uwezo wataalamu wa afya ili kuendeleza huduma hizo hata baada ya mradi kukamilika.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Wizara ya Afya Dkt. Greater Mande amesema mtoto wa jicho ni miongoni mwa sababu zinazosababisha upofu kwa wananchi wengi, kupitia kambi hiyo wagonjwa wengi wamepata fursa ya kurejeshewa uwezo wao wa kuona na kuendelea na shughuli zao za kila siku.

Pia, Dkt. Mande amewahimiza wananchi watakaonufaika na huduma hizo kuwa mabalozi kwa jamii zao kwa kutoa taarifa kwa watu wengine wenye changamoto za macho ili waweze kujitokeza kupata matibabu wanapopata fursa hiyo.

Nae, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Tabora Dkt. Boniface Marwa amesema wataendelea kushirikiana na wadau ili huduma hiyo ya upasuaji na mtoto wa jicho inakua endelevu na wananchi waendelee kupata huduma hizo pamoja na kuwashukuru Helen Keller kwa kuwasimesha wataalam wa eneo hilo. 

Sambamba na hilo, Mkurugenzi wa Shirika ka Helen Keller International Dkt. Geogle kabona amesema msaada huo utaendelea kutolewa pamoja na kutoa huduma ya mafunzo kwa wataalamu wa eneo hilo pamoja na kutolewa kwa elimu ili jamii ipate uelewa huo. 

"Tutaendelea kushirikiana na Serikali katika juhudi za kupunguza upofu unaozuilika na kuhakikisha wananchi wengiz zaidi wanaoata huduma bira za afya ya macho," amesema Dkt. Kabona.







Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Ujerumani (GIZ) zimesaini makubaliano ya utekelezaji wa mradi wa Digital Transformation Centre (DTC) Tanzania, hatua inayolenga kuimarisha matumizi ya teknolojia za kidijitali katika kukuza usawa wa kijinsia na maendeleo jumuishi nchini.

Makubaliano hayo yanaendeleza ushirikiano wa muda mrefu kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Shirikisho la Ujerumani kupitia GIZ, kwa lengo la kutumia teknolojia za kisasa kukabiliana na changamoto za kijamii na kiuchumi huku yakihakikisha wanawake na wasichana wanashiriki kikamilifu katika uchumi wa kidijitali unaokua kwa kasi.

Mradi wa DTC Tanzania unaendana na vipaumbele vya maendeleo vya taifa, ikiwemo Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Sera ya Taifa ya Jinsia na Maendeleo ya Wanawake ya mwaka 2023, Mpango wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto pamoja na Mfumo wa Kimkakati wa Uchumi wa Kidijitali wa Tanzania wa mwaka 2024–2034.

Akizungumza wakati wa hafla ya kusaini makubaliano hayo, Mkurugenzi Mkazi wa GIZ nchini Tanzania, Anne Hahn, alisema kuwa teknolojia za kidijitali zimekuwa nyenzo muhimu katika kuwawezesha wanawake kupata ujuzi wa kiufundi na ujasiriamali unaowawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi na maendeleo ya jamii.

Hahn alisema kuwa wanawake wanapopata fursa ya kutumia teknolojia za kidijitali, huongeza uwezo wao wa kubuni suluhisho mbalimbali, kuanzisha biashara, kuzalisha ajira na kuchangia kwa kiwango kikubwa ukuaji wa uchumi wa taifa. Alibainisha kuwa uwekezaji katika teknolojia unafungua milango mipya ya fursa kwa wanawake na wasichana katika nyanja mbalimbali za maendeleo.

“Wanawake wanapowezeshwa kutumia teknolojia za kidijitali, wanakuwa wabunifu, wajasiriamali na washiriki muhimu katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii ya nchi,” alisema Hahn, akisisitiza kuwa ushiriki wao katika sekta ya teknolojia ni muhimu kwa maendeleo endelevu na jumuishi.

Aidha, ametoa wito wa kuendelea kuwekeza katika mafunzo ya ujuzi wa kidijitali na programu za ujasiriamali kwa wanawake na wasichana ili kuhakikisha wanapata fursa zinazotokana na mageuzi ya teknolojia duniani, huku akieleza kuwa uwezeshaji wa wanawake kupitia teknolojia si suala la usawa wa kijinsia pekee bali ni msingi muhimu wa kukuza ubunifu, ajira na ukuaji wa uchumi wa taifa.







Jane Mwakyoma, Nkasi -Rukwa.

WILAYA ya Nkasi mkoani Rukwa imeanza kuweka mikakati mbalimbli ya kukabiliana na ugonjwa wa Ebola kwa kutoa elimu kwa wananchi namna ya dalili zake na njia za kujikinga na ugonjwa huo.

Kaimu mkuu wa wilaya ya Nkasi ambaye pia ni mkuu wa wilaya ya Sumbawanga Nyakia Chirukile amezitaka Taasisi zote zinazotoa huduma kwa jamii kuhakikisha zinatoa elimu kwa wananchi kuhusu dalili za ugonjwa wa Ebola na njia za kujikinga na kuwa tayari kuchukua hatua endapo kutatokea mshukiwa wa Ebola.

Akizungumza katika kikao cha dharura cha kamati ya Afya ya msingi wilaya (DPHC) Chirukile amesema wilaya imeanza kampeni ya uhamasishaji kwa kuwashirikisha wadau mbalimbli wa Afya, Elimu, Dini na maofisa maendeleo ya jamii kutoka ngazi za vijiji mpaka wilaya ili kuhakikisha elimu ya ugonjwa wa Ebola inazifikia jamii zote.

“Nimewaita hapa makundi yote katika jamii, tuzijue dalili na jinsi ya kujikinga na Ebola lakini pia kutoa elimu kwenye jamii na kuweka mikakati ya kuchukua kama Wilaya hasa tunapopata wagonjwa na kupokea wageni katika Wilaya yetu”amesema Chirukile.

Aidha Ofisa Afya wa wilaya ya Nkasi Method Mwankejela amesema Zahanati za Kipili, Kizumbi, Namanyere, Kabwe na Justice Korongwe zimetengwa kwa ajili ya kupokea na kuhudumia wagonjwa wanaoshukiwa na ugonjwa huo.

Mwankejela amesema mpaka sasa hakuna mgonjwa anayeshukiwa kuambukizwa na ugonjwa wa Ebola na kuwataka wananchi kuendelea kuchukua tahadhari kwa wageni wanaoingia na kutoka nchini.

Kwa upande wao Sheikh Mustapha Lupa na Mchungaji Fidelis Maheke ambao ni wajumbe wa kamati ya amani ya wilaya ya Nkasi wameipongeza serikali kwa kuanzisha mkakati wa kukabiliana na mlipuko wa ugonjwa hatari wa ebola ambapo wamesisitiza elimu kutolewa ya kutosha hasa maeneo ya mwambao mwa ziwa kama kabwe,korongwe,kirando,kala,Namansi na maeneo mengine ili jamii iweze kujikinga vyema na ugonjwa wa Ebola.








KUTOKA RUKWA.

HALMASHAURI ya Manispaa ya Sumbawanga na Halmashauri ya Mji Tunduma zimeendelea kuimarisha ushirikiano wa kiutendaji kupitia ziara ya mafunzo iliyolenga kubadilishana uzoefu wa utoaji huduma kwa wananchi, usimamizi wa miradi ya maendeleo na uhifadhi wa mazingira kwa manufaa ya wananchi na maendeleo ya Taifa kwa ujumla.

Timu ya Uongozi na Wataalamu kutoka Halmashauri ya Mji Tunduma imefanya ziara hiyo katika Manispaa ya Sumbawanga Mkoani Rukwa ikiongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Momba Elias Mwandobo akiambatana na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Tunduma Salum Kiyambi, Mkurugenzi wa Halmashauri Mariam Chaurembo, Waheshimiwa Madiwani pamoja na wataalamu kutoka sekta mbalimbali.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo Mwandobo amesema kubadilishana uzoefu kati ya Halmashauri ni njia muhimu ya kuongeza ufanisi wa utendaji kazi na kuharakisha maendeleo ya wananchi kwa kujifunza mifano ya mafanikio inayotekelezwa katika maeneo mbalimbali Nchini.

Katika ziara hiyo wajumbe wametembelea miradi mbalimbali ya kimkakati inayotekelezwa katika Manispaa ya Sumbawanga ikiwemo Mradi wa Soko la Kimataifa la Mazao Kanondo, Chuo cha Ufundi Stadi (VETA) Rukwa pamoja na Uwanja Mpya wa Ndege wa Sumbawanga ambao rasmi ulianza kutumika Juni 10, 2026 kwa safari za ndege kuelekea Tabora na Dar Es Salaam.


Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imesaini hati tatu za makubaliano ya ushirikiano wa kielimu na Urusi zitakazowezesha kubadilishana wataalamu, kuendeleza tafiti za pamoja na kuongeza fursa za elimu ya juu kwa wanafunzi wa nchi hizo mbili.

Akitoa taarifa hiyo kwa Waandishi wa Habari Juni 10, 2026 jijini Dodoma Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda amesema hatua hiyo imefikiwa baada ya ziara ya kihistoria nchini humo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ambayo imeleta mafanikio katika nyanja za elimu, sayansi na teknolojia 

Waziri Mkenda ametaja makubaliano yaliyofanyika ya kwanza ni kati ya Wizara ya Elimu ya Tanzania na Wizara ya Elimu ya Urusi yanayolenga kubadilishana walimu na wataalamu, kuendesha semina za pamoja na kufundisha lugha za Kiswahili na Kirusi.

Makubaliano ya pili ambayo Wizara imeingia yamehusisha Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam (DIT) na Chuo Kikuu cha RUDN, ambapo wanafunzi wa kitanzania watapata fursa ya kusoma shahada ya kwanza ya Teknolojia ya Anga kupitia mfumo wa shahada pacha, wakisoma miaka miwili Tanzania na miaka miwili nchini Urusi

“Kupitia programu hii, wanafunzi watatumia mtaala wenye viwango vya kimataifa, kusoma kwa lugha ya kingereza nchini Tanzania na kujifunza lugha ya Kirusi kabla ya kuendelea na masomo yao nchini Urusi. Hatua hii itaongeza uwezo wa taifa katika sayansi, teknolojia na uhandisi.” Amesema Waziri Mkenda

Hati ya tatu ya makubaliano kati ya DIT na Chuo Kikuu cha RUDN inalenga programu za shahada ya uzamili, ambapo wanafunzi watapata nafasi ya kusoma katika nchi zote mbili na kutunukiwa shahada zinazotambulika kimataifa, huku ushirikiano huo ukifungua milango mipya ya utafiti na ubunifu.

"Chuo Kikuu cha RUDN kimeahidi kutoa ufadhili wa masomo (scholarships) kumi kwa wanafunzi wa Kitanzania. Ufadhili huu, utawawezesha Watanzania kusoma nje ya nchi kupitia mpango wa Samia Scholarship Extended DS/AI+" amesema Prof Mkenda.

Mafanikio  haya yanafuatia ziara ya kihistoria ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, nchini Urusi mapema mwezi huu yakilenga kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia, kiuchumi na kielimu kati ya Tanzania na Urusi, huku akipata heshima ya kutunukiwa Shahada ya Udaktari wa Heshima kutoka Chuo Kikuu cha RUDN, kutambua mchango wake katika uongozi na maendeleo ya kimataifa.







Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma 

Soko la ajira nchini Tanzania limeendelea kuimarika, baada ya kiwango cha ukosefu wa ajira kushuka hadi asilimia 6.2 mwaka 2024, ikilinganishwa na asilimia 8.7 iliyorekodiwa mwaka 2020/21.

Hayo yamebainishwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, wakati akiwasilisha Bungeni Taarifa ya Hali ya Uchumi wa Taifa kwa mwaka 2025 pamoja na Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa mwaka 2026/27.

Profesa Mkumbo amesema hali hiyo ni ishara ya kuimarika kwa mazingira ya biashara, uwekezaji na uzalishaji nchini, hali inayochochea ongezeko la nafasi za ajira katika sekta mbalimbali.

Kwa mujibu wa takwimu hizo, kasi ya ukuaji wa ajira pia imepanda kwa kiwango kikubwa, ambapo wastani wa ukuaji wa ajira kwa mwaka umefikia asilimia 7.8 mwaka 2024, kutoka asilimia 2.3 mwaka 2020/21.

Aidha, nguvu kazi nchini imeongezeka na kufikia watu milioni 27.3, sawa na asilimia 73.2 ya wananchi wote wenye uwezo wa kufanya kazi, ikilinganishwa na asilimia 72.1 ya mwaka 2020/21.

Kati ya nguvu kazi hiyo, takriban watu milioni 25.6 wanajishughulisha na shughuli za kiuchumi zinazowaingizia kipato, hali inayoonyesha ushiriki mpana wa wananchi katika uzalishaji.

Kwa upande wa sekta, kilimo kinaendelea kuwa mwajiri mkubwa zaidi nchini kwa asilimia 54.2, kikifuatiwa na sekta ya huduma yenye asilimia 35.5, huku sekta ya viwanda ikichukua asilimia 10.3 ya ajira zote.

Serikali imesema mafanikio hayo yametokana na juhudi za kuboresha mazingira ya biashara, kuvutia uwekezaji na kuimarisha shughuli za uzalishaji katika sekta mbalimbali za uchumi.

Kwa ujumla, mwenendo huo unaonyesha mwanga mpya katika soko la ajira nchini, huku matarajio yakiwa ni kuendelea kupungua kwa ukosefu wa ajira na kuongezeka kwa fursa zaidi kwa wananchi katika miaka ijayo.



Na mwandishi wetu, Zanzibar.

Katika  kuunga mkono juhudi za serikali ya awamu ya sita  la kukuza uchumi kwa wananchi wake  Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya imeamua mpango  kabambe ya kuhakikisha inaboresha soko lake la bidhaa pamoja na huduma mbalimbali lililopo katika Mji wa Mbalizi Tarafani ili kuchochea zaidi shughuli za kiuchumi na kuongeza hali ya ukusanyaji wa mapato kwa ajili ya kuharakisha   kwa  kuleta mabadiliko chanya ya kimaendeleo.

Mpango huo umekuja kufuatia ziara ya baraza la madiwani pamoja na jopo la wataalam kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, waliozuru visiwani Zanzibar, kuanzia tarehe 01 hadi 04 Juni 2026, kwa ajili ya mafunzo mbalimbali kuhusu mifumo ya uongozi katika sekta ya uchumi na kijamii kwa ajili ya kuleta maendeleo kwa wananchi kupitia fursa zinazowazunguka katika maeneo yao husika ya kiutawala.

Ziara hiyo ya mafunzo ilifanyika katika Baraza la Manispaa ya Magharibi B, inayoongozwa na Mkurugenzi Mtendaji, Bi. Sabra Issa Machano, ambapo ugeni wa baraza la madiwani na wataalam wanaounda menejimenti ya Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, walipata fursa ya kutembelea masoko makubwa mawili: Soko la Mwanakwerekwe na Soko la Jumbi.

Soko la Mwanakwerekwe ni soko lilijengwa baada ya kushirikisha wadau pamoja na uwezeshaji kupitia mkopo kutoka sekta binafsi kisha baadae serikali kuu kutoa fedha kwa ajili ya kumaridhia mradi huo.

Soko hilo linabeba wafanyabiashara takribani 5,224 tofauti na awali kabla ya kuboreshwa, ambapo lilikuwa linabeba wafanyabiashara 3,000 pekee. Uboreshaji huo umevutia karibu asilimia 50 ya wafanyabiashara wapya.

“Soko hili linafanya kazi saa 24 na linahudumia takribani watu 50,000 kwa siku. Ujenzi wake umezingatia kila aina ya watu kulingana na mahitaji yao. Hapa kuna maduka 187, vibanda 1,344, meza 152, bucha 18, maghala 12, vibanda vya kuegesha kwa biashara maarufu kama vigoli 56,” ameeleza Mkurugenzi Mtendaji wa Baraza la Manispaa ya Magharibi B.

Mfumo huo umewavutia zaidi madiwani pamoja na timu ya wataalam wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, waliokuwa katika ziara hiyo na kuweka azimio la kutaka kuboresha soko la Mbalizi, ambalo limekuwa kitovu kikubwa cha kibiashara katika Halmashauri. Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, Bi. Erica E. Yegella amesema Halmashauri inahitaji kuwa na soko la kisasa kama Mwanakwerekwe na Jumbi kwa ajili ya ustawi wa uchumi wa Halmashauri na wananchi wake.

Ameeleza kwamba Halmashauri inakusanya mapato ya ndani takribani shilingi bilioni nane (8) kwa mwaka, lakini ipo fursa ya kuboresha soko la Mbalizi hata kwa kupitia ubia na wadau wa maendeleo kutoka sekta binafsi ikiwemo taasisi za kifedha kama vile benki kwa ajili ya kuboresha soko hili linalobeba kiwango kikubwa cha wajasiriamali wakiwemo vijana wa kike na kiume sambamba na wanawake.

“Ziara yetu Zanzibar imekuwa na manufaa makubwa. Sote kama menejimenti na baraza letu la madiwani tumejionea kwa macho. Ipo fursa ya kuongeza mapato kupitia soko letu. Kinachotakiwa ni kuboresha miundombinu ya soko letu. Tuko tayari kuingia ubia na mdau yoyote ambaye anaweza kushirikiana nasi katika kuboresha sehemu hii kwa ajili ya kutengeneza mazingira rafiki ya biashara kwa wajasiriamali wetu.” Amesema Mkurugenzi Mtendaji Bi. Erica E. Yegella.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, Mhe. Aidda C. Haule, amesema Mji wa Mbalizi unakua kwa kasi kutokana na muingiliano mkubwa wa watu kupitia biashara mbalimbali. Amesema ujenzi wa masoko ya kisasa kama ilivyo kwa Zanzibar itasaidia pia kuhakikisha suala la mipango miji linazingatiwa kikamilifu pasina changamoto tofauti na ilivyo sasa, ambapo wafanyabiashara wametapakaa mpaka barabarani hali inayoleta usumbufu kwa watembea kwa miguu na watu wanaoendesha vyombo vya moto.

“Ziara hii imekuwa na tija kwetu kama Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya imetuonesha namna ambavyo tunaweza kushirikiana na wadau kuboresha masoko yetu, ambayo ni vituo muhimu kibiashara. Lakini pia tunaweza kuweka mazingira rafiki kwa wafanyabiashara pamoja na watoto wao kwa kujenga hata miundombinu ya kulelea watoto ndani ya soko letu kama ambavyo tumeona katika masoko ya hapa Zanzibar.” amesema Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya.

Halmashauri Wilaya ya Mbeya imemaliza ziara yake ya siku nne ambapo imewea kutembelea maeneo mbali mbali yaliyopo Visiwani Zanzibra ikiwemo eneo la unguja ambapo madiwani, wataalamu pamoja na Mkurugenzi wameweza kujifunza mambo mbali mbali  ambayo yataweza kuwa ni moja ya mkombozi mkubwa  katika utekelezaji wa majukumu yao ikiwemo suala la utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa wananchi.





Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi na wadau mbalimbali wa sekta ya afya ili kuimarisha utoaji wa huduma bora za matibabu kwa wananchi.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 11 Juni 2026, Ikulu Zanzibar, alipokutana na ujumbe wa Taasisi ya Humaniti ukiongozwa na Mtendaji Mkuu wake, Bw. Firaaz Azeez, pamoja na Mwanzilishi wa Doris Mollel Foundation, Bi.  Doris Mollel.

Amesema Serikali inathamini mchango wa Taasisi ya Humaniti katika kuimarisha sekta ya afya kupitia uwekezaji katika rasilimali watu, miundombinu na vifaa tiba, huku akisisitiza umuhimu wa kuimarisha mifumo endelevu ya afya badala ya kutegemea programu za muda mfupi.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi ameishukuru Taasisi ya Doris Mollel Foundation kwa juhudi zake za kusaidia huduma za afya kwa watoto wachanga na watoto wanaozaliwa kabla ya wakati, hatua inayochangia kuokoa maisha ya watoto hao.

Katika hatua nyingine, Taasisi ya Humaniti imemkabidhi Rais Dkt. Mwinyi hundi ya shilingi milioni 503 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba vya uchunguzi na matibabu ya magonjwa ya moyo kwa watoto.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Humaniti, Bw. Firaaz Azeez, amepongeza maendeleo makubwa ya sekta ya afya Zanzibar baada ya kutembelea Hospitali za Lumumba, Chumbuni na Magomeni.

















Top News