Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Shirikisho ya Somalia wamesaini Hati ya Makubaliano kuhusu masuala ya kiuhamiaji.

Hati hiyo ya Makubaliano imelenga kuondoleana hitaji la visa kwa Pasipoti za kidiplomasia na za kiutumishi pamoja na mashirikiano katika masuala ya uhamiaji baina ya nchi hizo mbili.

Hati hiyo ya Makubaliano imesainiwa leo jijini Dar es Salaam na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,Patrobas Katambi na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi wa Serikali ya Somalia,Jenerali Abdullahi Sheikh Ismail Fartaag.

Akizungumza baada ya kusaini Hati ya Makubaliano , Waziri Katambi ametambua ushirikiano uliopo kati ya nchi hizo pamoja na mashirikiano yaliyopo katika masuala ya usalama wa raia na kuhamisha wafungwa.

Vilevile Waziri Katambi ameeleza kuwa  Tanzania itaendeleza ushirikiano na nchi zilizopo katika Jumuiya ya Afrika Mashariki kuhakikisha usalama na Amani vinatawala katika ukanda wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Tukio hilo pia limehudhuriwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,Ayoub Mohamed Mahmoud na Katibu Mkuu,Ally Senga Gugu.







-Pia awasilisha Salamu za Pole za Rais Dkt. Samia kwa waliofariki kwenye Machimbo, Korogwe.

Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amehani msiba wa Idrissa Zubeir Bin Ali (58) ambaye ni mdogo wake Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania Dkt. Abubakary Zubeiry bin Ally ambae amefariki Februari 15, 2026 katika Hospitali ya Muhimbili Dar Es salaam.

Akiwa Msibani hapo kuhani msiba huo, Mhe. Dkt. Mwigulu amewasilisha salamu za pole kwa wanakorogwe kutoka kwa Rais Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa vifo watu watano vilivyotokea Februari 15, 2026 katika Machimbo ya Mchanga ya BOLBIT kijiji cha Makuyuni, Tarafa ya Mombo.

“Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan anawapa pole na kuwaombea moyo wa subira ndugu, Jamaa na wafiwa na Mwenyezi Mungu awape Pumziko la Amani marehemu wote”.





-Ni wa vifaa vya ujenzi jengo la Halmashauri ya Wilaya

-Zimo nondo 700, Marine boards 500 na matofali 2,000

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba ameagiza wajumbe wa Kamati Mapokezi na Kamati za Ujenzi za mradi wa ujenzi wa ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Muheza wakamatwe na kuhojiwa mara moja ili watoe taarifa juu ya upotevu wa vifaa vya mradi huo.

“Kuna nondo 700, Marine boards 500 na matofali 2,000... hivi vifaa havijulikani viko wapi. Wahusika kila siku mnaripoti kazini, na mishahara mnalipwa wakati ujenzi umesimama na hakuna hatua zinazochukuliwa,” amesema wakati akimhoji Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Dkt. Jumaa Mhina.

Ametoa agizo hilo leo (Jumatatu, Februari 16, 2026) wakati akizungumza na wananchi wa Lusanga, kata ya Mgomeni, wilayani Muheza waliofika kushuhudia uwekaji wa jiwe la msingi la ofisi hiyo itakayokuwa na ghorofa moja pindi ikikamilika.

“Kamanda wa TAKUKURU ninahitaji hii taarifa kwa kina kabla sijamaliza ziara yangu mkoani Tanga. OCD fuatilieni kwa kina ushiriki wa watumishi wa hii Halmashauri. Kila mmoja ahojiwe hadi tujue vifaa vilipoteaje.”

Amesema kuwa anazo taarifa kwamba timu ya manunuzi imenunua vifaa ambavyo vimewekwa stoo wakati hatua yake ya ujenzi haijafikiwa. “Nimeambiwa vifaa vingine vimekuja lakini vimekaa stoo tu. Ni kwa nini mmenunua vifaa hivyo wakati hamjamaliza hatua ya kwanza? Mshauri mwelekezi wa mradi yupo lakini hamsikilizi ushauri anaotoa,” alisema.

Jengo hilo ndiyo limemalizika kujengwa ghorofa ya chini, na linasubiri kuanza kuwekewa linta kwenye ghorofa ya kwanza.

Waziri Mkuu amekemea tabia ya kutochukua hatua masuala kama hayo yanapojitokeza hasa ikizingatiwa kwamba Halmashauri nyingine ambazo walipewa fedha kwa wakati mmoja wao wameshakamilisha kazi ya ujenzi.

Mapema, akitoa taarifa ya ujenzi wa mradi huo, Kaimu Mkuu wa Idara ya Miundombinu na Maendeleo Mijini na Vijijini, Mhandisi Abdalla Jaha alisema mradi huo ambao umefikia asilimia 68, ulianza kujengwa Septemba 29, 2023 na wanatarajia ifikapo mwishoni mwa Juni, 2026 sakafu ya chini ianze kutumika.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ametoa pongezi kwa kiwanda cha vifungashio cha Yogi PolyPack ambacho kiko Pongwe, nje kidogo ya Manispaa ya Tanga.

Akizungumza na viongozi na watumishi wa kiwanda hicho, Waziri Mkuu amesema uwekezaji uliofanywa ni mkubwa na kwamba serikali itaendelea kuhakikisha inatengeneza mazingira mazuri ya uzalishaji.

“Nimetembelea kiwanda, nimeona kazi nzuri ikiendelea na inatumia teknolojia ya kisasa. Haya ndiyo mambo Mheshimiwa Rais anataka kuyaona. Unatengeneza ajira, unazalisha bidhaa ambazo ni malighafi kwa viwanda vyetu hapa nchini na unatoa kipato kwa wafanyakazi wako,” amesema.

Mapema leo, Waziri Mkuu alitembelea bandari ya Tanga na kukagua shughuli za bandari hiyo na kisha kuzungumza na watumishi.

Akiwa bandarini hapo, alipokea maelezo ya uboreshaji wa bandari hiyo kisha akatembelea eneo ambalo zitajengwa gati mbili mpya, katika bandari ya Tanga ikiwa ni mkakati wa Serikali ya kuiongezea uwezo bandari ya Tanga wa kutoa huduma shindani na za ufanisi.

Akizungumza na watumishi wa bandari ya Tanga, Waziri Mkuu aliahidi kwamba Serikali itahakikisha inaendelea kufanyia kazi changamoto zote za kiutumishi zinazowahusu watumishi hao.

“Serikali itaendelea kufanya maboresho katika bandari hii ili iweze kuhudumia idadi ya meli nyingi kwa kadiri inavyowezekana. Tunatambua ushindani wa kibiashara uliopo lakini tutaendelea kufanya maboresho ili tunufaike na nafasi ya kijiografia ya mkoa wetu,” alisema.

Pia ameiagiza Mamlaka ya Bandari ifanyie kazi changamoto ya uhaba wa vifaa vya kupakulia mizigo ili kuendana sambamba na maboresho hayo.






MKUTANO wa Waandishi wa Habari kuhusu Ziara za Kikazi alizofanya Rais Mhe. Dkt. Samia, Jijini Addis Ababa nchini Ethiopia pamoja na Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), Ikulu Jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Bw. Bakari Machumu akizungumza na Waandishi wa Habari, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 16 Februari, 2026 kuhusu Ziara za Kikazi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, alizofanya Jijini Addis Ababa nchini Ethiopia tarehe 12-15 Februari, 2026 pamoja na Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) tarehe 2-6 Februari, 2026.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mahamoud Thabit Kombo akizungumza na Waandishi wa Habari, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 16 Februari, 2026 kuhusu mafanikio ya Ziara ya Kikazi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, aliyofanya Jijini Addis Ababa nchini Ethiopia tarehe 12-15 Februari, 2026. Waziri Mhe. Balozi Kombo alielezea kwa kina ushiriki wa Tanzania katika mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU) pamoja na mafanikio yaliyopatikana katika mkutano huo.
Viongozi mbalimbali waliohudhuria Mkutano wa Waandishi wa Habari, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 16 Februari, 2026 kuhusu Ziara za Kikazi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, alizofanya Jijini Addis Ababa nchini Ethiopia tarehe 12-15 Februari, 2026 pamoja na Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) tarehe 2-6 Februari, 2026.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Dkt. Seif Shekalaghe akizungumza na Waandishi wa Habari, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 16 Februari, 2026 kuhusu mafanikio ya Ziara ya Kikazi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, aliyofanya Jijini Addis Ababa nchini Ethiopia tarehe 12-15 Februari, 2026.




Waandishi wa Vyombo mbalimbali vya Habari wakiwa kwenye Mkutano kuhusu Ziara za Kikazi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, alizofanya Jijini Addis Ababa nchini Ethiopia tarehe 12-15 Februari, 2026 pamoja na Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) tarehe 2-6 Februari, 2026.



Na Saidi Lufune, Dodoma
NAIBU  Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Hamad Hassan Chande (Mb), amehimiza Idara ya Maliakale kuongeza ubunifu katika kutangaza vivutio vya maliakale na makumbusho ya kihistoria ili kuvutia watalii wengi wa ndani na nje ya nchini.

Mhe. Chande amebainisha hayo jijini Dodoma katika kikao kazi na Idara ya Malikale ambapo amefafanua kuwa sekta ya maliakale nchini inapaswa kuwa juu na kuwa sehemu ya kuchangia ukuaji wa mapato katika ukuaji wa uchumi wa Taifa hususan katika kufufua maeneo mapya ya utalii wa malikale na makumbusho ya kihistoria

Aidha, ameiagiza idara hiyo kuongeza mashirikiano yenye tija na Wizara ya Utalii na Mambo ya Malikale ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) ili kuongeza nguvu katika kutangaza mazao mapya ya vivutio vya Maliakale huku akisisitiza uhifadhi wa makumbusho ya nyimbo zitokananazo na matukio ya historia ya Taifa wakati na baada ya ukombozi wa Tangangika na Zanzibar.

Awali akiwasilisha taarifa za idara hiyo, Mkurugenzi wa Idara ya Malikale Dkt. Christowaja Ntandu amebainisha kuwa Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Idara ya Maliakale itaendelea kuhamasisha Mamlaka za Serikali za Mitaa kufungua maeneo na vivutio vipya vya Malikale; kuendelea kutangaza na kuhamasisha jamii kupitia maonesho, matamasha na warsha juu ya umuhimu wa kuwekeza na kutumia rasilimali za utamaduni kama zao mojawapo la utalii hapa nchini.






TUME ya Uchunguzi wa Matukio ya Uvunjifu wa Amani yaliyojitokeza wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, imeendelea na vikao vyake leo Februari 16, 2026 kwa kukutana na Katibu Mkuu Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Dkt Faraji Mnyepe na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi Ally Gugu.

Mkutano huo wa Tume na Makatibu Wakuu hao umefanyika katika ukumbi wa Tanganyika uliopo jengo la Benki Kuu ya Tanzania (BoT) mkoani hapa, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Tume kukusanya taarifa, maoni na ushauri kutoka kwa viongozi mbalimbali.

Katika mkutano huo hoja zilizojadiliwa zilihusu maeneo ya tathmini ya athari za matukio hayo na ushauri wa hatua za kijamii na kisheria zinazoweza kuchukuliwa ili kuimarisha amani na mshikamano wa kitaifa.

Tume inaendelea kukutana na makundi mbalimbali ikiwemo waathirika wa matukio ya uvunjifu wa amani katika mikoa tofauti nchini, kwa lengo la kukusanya ushahidi na taarifa zitakazoiwezesha kuandaa ripoti ya kina.







Mbunge wa jimbo la Kibamba,Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki ameshiriki Baraza la Wazazi Wilaya ya Ubungo kama Mgeni Rasmi, ambapo amewashukuru wajumbe wa jumuiya hiyo kwa mchango wao mkubwa katika kukipambania Chama Cha Mapinduzi wakati wa Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025.

Katika hotuba yake, Mheshimiwa Kairuki aliwapongeza wazazi kwa ushindi mkubwa wa asilimia 97% waliompatia Samia Suluhu Hassan, na kuwasilisha salamu nyingi kutoka kwake kwenda kwa Jumuiya hiyo. Alieleza kuwa ushindi huo ni ishara ya mshikamano, uaminifu na juhudi za pamoja katika kuimarisha Chama na Taifa kwa ujumla.

Aidha, aliwakumbusha wazazi wajibu wao wa kuendelea kuwa walezi bora kwa vijana. Alisisitiza umuhimu wa wazazi kukaa na watoto wao, kuwalea katika maadili mema, na kuwaandaa kuwa viongozi bora wa kesho watakaolisukuma mbele Taifa.

Katika mkutano huo, Jumuiya ya Wazazi Wilaya ya Ubungo iliwasilisha changamoto ya ujenzi wa nyumba ya mtumishi wa jumuiya hiyo (Katibu wa Wazazi Wilaya), wakieleza kuwa ukosefu wa makazi rasmi unakwamisha utendaji kazi wa kila siku. Baada ya kupokea ombi hilo, Mheshimiwa Kairuki aliguswa na changamoto hiyo na kuahidi kuchangia shilingi milioni kumi (10,000,000) kama mwanzo wa ujenzi wa nyumba hiyo.

Pia aliwapongeza kwa uwekezaji wao wa kujenga Ofisi ya Jumuiya ya Wazazi Wilaya ya Ubungo, akiahidi kuendelea kushirikiana nao katika kuimarisha jumuiya hiyo na kuendeleza maendeleo ya Wilaya.

Akihitimisha hotuba yake, Mheshimiwa Kairuki alipiga goti kama ishara ya shukrani na heshima kwa wazazi, akiwashukuru kwa moyo wao wa kujitolea na uaminifu wao kwa Chama na Taifa.


 

 


MWANASHERIA Mkuu wa Serikali, Hamza Johari amewaongoza Mawakili wa Serikali kutoa huduma za ushauri wa Kisheria kwa wananchi wakati wa Kliniki ya Sheria bila malipo iliyozinduliwa tarehe 16 Februari, 2026 katika Viwanja vya Mnazi Mmoja Jijini Dar es Salaam.

Johari amemuhudumia mwananchi aliyekuja kupata huduma ya ushauri wa kisheria ambapo alimsikiliza na kumuhudumia Sarah Mohamed aliyewasilisha malalamiko yake kuhusiana changamoto ya mirathi inayomkabili.

“Tumeyapokea malalamiko yako na mimi pamoja na timu tutayafanyia kazi kwa haraka ili kuweza kutatua changamoto inayokukabili”. Amesema Mwanasheria Mkuu wa Serikali

Katika zoezi hilo la kutoa huduma kwa wananchi Mwanasheria Mkuu wa Serikali aliambatana na Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Zainab Katimba.

Timu ya Mawakili wa Serikali kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali imepiga kambi katika Viwanja vya Mnazi Mmoja Jijini Dar es Salaam kutoa huduma mbalimbali za kisheria bila malipo kwa wananchi wa mkoa wa Dar es Salaam kuanzia tarehe 16 hadi 22 Februari, 2026.

Na Oscar Assenga, TANGA

WAZIRI Mkuu Dkt Mwigulu Nchemba amefanya ziara ya kutembelea utekelezaji wa mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki unaotekelzwa eneo la Chongoleani Jijini Tanga huku akiridhishwa na kasi ya utekelezaji wake unaoendelea kwa kuzingatiwa viwango vilivyowekwa.

Nchemba aliyasema hayo wakati akizungumza katika ziara yake eneo la Chongoleani Jijini Tanga linapoishia Bomba la Mafuta ambalo litasafirisha mafuta kutoka Hoima nchini Uganda hadi eneo la Chongoleani licha ya kuwepo kwa changamoto zilizojitokeza wakati wa utekelezaji wake.

Alisema kwamba kwamba mradi huo wa kimkakati ambao utagharimu Dola za Marekani Bilioni 5.65 ni kielelezo cha Undugu Kati ya Tanzania na Uganda ambapo mradi huo umefikia asilimia 81 ya utekelezaji wake

Ambapo alisema changamoto hizo ni pamoja na mlipuko wa ugonjwa wa Uviko 19 pamoja na mtikisiko wa uchumi wa dunia lakini akabainisha kuwa hatua zilizochukuliwa zimewezesha mradi huo kuendelea bila kuathiri ubora na malengo yake.

"Mradi umepiga hatua lakini wakati wa utekelezaji wa mradi huu kulikuwepo na changamoto ikiwemo dunia kupita kwenye misikusuko ya kiuchumi na mabadilio ya sera za kiuchumi lakini umeendelea kutekelezwa kwa kasi jambo ambalo linaendelea kuipa heshima nchi yetu pamoja na ndugu zetu tunaotekeleza mradi huo kwa pamoja "Alisema

Mradi huo wa EACOP una urefu wa takribani Kilomita 1,444 ukianzia Hoima nchini Uganda hadi Chongoleani Tanzania na unatarajiwa kusafirisha mafuta ghafi kutoka maeneo ya uzalishaji ya Uganda hadi kwenye Kituo cha Kuhifadhi na Kusafirisha mafuta eneo la Chongoleani Jijini Tanga.


Alisema kwamba mradi huo unatajwa kuwa miongoni mwa miradi mikubwa ya kimkakati katika ukanda wa Afrika Mashariki ukilenga kuchochea ukuaji wa uchumi na kuongeza ajira kwa wananchi pamoja na

Aidha Waziri Mkuu huyo aliwatahadharisha watu wanaoanzisha makampuni na kuyaita ya wazawa huku yakiwa yanamilikiwa na wageni ili kunufaika na fursa ya “Loal Content” ya ushirikishwaji wa watanzania mradi kwamba watakapogundulika watafungiwa na hawatafanya kazi tena hapa nchini kwani hivyo ni kuwatapeli watanzania na kuwaibia fursa


Awali akizungumza katika ziara hiyo,Naibu Waziri wa Nishati Salome Makamba alisema kwamba katika mradi huo ulianza mwaka 2022 na unatarajiwa kukamilika Julai 2026 huku akieleza Serikali kwa kushirikiana na EACOP imekamilisha zoezi la kuthamini na utwaaji wa ardhi ya mradi.

Alisema kwamba hadi kufikia Januari 2026 Jumla ya Sh. Bilioni 35.06 zimetumika kulipa stahiki ya fidia kwa wananchi 9,869 kati ya wananchi 9,927 sawa na asilimia 96.4 kwa wanaopisha eneo la mradi na mkoani Tanga wananchi 1,688 wamefidiwa na kulipwa Jumla ya Bilioni 10.49.

Aidha alisema wananchi 294 wamenufaika kwa kujengewa nyumba 340 za makazi mbadala na wameshakabidhiwa nyumba zao hapa Tanga walionufaika ni wananchi 43.

Alisema kwamba wananchi wa Mkoa wa Tanga waliopatiwa udhamani wa chakula ni 1,200 huku wananchi 191 wameshiriki mafunzo ya ufugaji wa kuku,nyuki na ujasiriamali ili kuongeza kipato.

Makamba alisema katika mkoa huo miundombinu iliyojengwa ni pamoja na kituo kimoja cha Afya na kituo kimoja cha kupunguza mgandamizi wa mafuta ghafi kilichopo Handeni,Matenki Mawili ya Kuhifadhia Mafuta yaliyopo Tanga na Gati ya kupakia mafuta na kituo kikuu cha kuongeza ulinzi wa bomba la mafuta.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Tanga Balozi,Dkt Batilda Burian alisema wana Tanga wanamshukruu Rais kwa jinsi ambavyo maono yake na Rais wa Uganda Yoweri Museveni kwamba mradi umekuwa mzuri na shughuli zimekwenda vizuri na wananchi wa Tanga wamepata ajira.


Alisema pia kwa waliopitiwa na mradi waliweza kupata fidia bila kuwepo kwa changamoto yoyote lakini waliweza kusaidiwa na mashamba yaliyoguswa waliweza kulimiwa huku akiwashukuru EACOP kuna maeneo walikwenda kwa sababu walikwenda na utaalamu wakarudi kumueleza kuna changamoto ya uharibifu wa panya wa mazao iliwasaidia nao kuwaeleza wizara na hivyo kuondosha changamoto hiyo.

Mkuu wa Mkoa alisema kwamba zaidi vijana wa Tanga wameweza kushirikiana na wahandisi na wanashukuru mradi upo salama na hawajapata changamoto yoyote ya watu kupata madhara na suala la mazingira kwa sababu mradi umekwenda kwenye bahari wamehakikisha maeneo yenye uoto asili waliweza kuzingatia na hata kuchepusha ili wasiharibu na wanazingatia mazingira ya bahari.




Top News