Na Oscar Assenga,TANGA

SERIKALI imekipongeza Chama cha Washauri wa Wanafunzi wa Vyuo Vikuu Tanzania (TACOGA) kwa kuendelea kuandaa mafunzo yanayolenga kuimarisha uwezo wa kitaaluma na kiutendaji wa washauri wa wanafunzi, wanasihi na viongozi wa serikali za wanafunzi kutoka vyuo mbalimbali nchini.

Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo yaliyofanyika jijini Tanga,Mkurugezi wa Maendeleo ya Jinsia kutoka Wizara ya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wanawake na Makundi Maalumu Badru Abdnur alisema mafunzo hayo yamekuwa jukwaa muhimu la kuwajengea washiriki uwezo wa kukabiliana na changamoto zinazowakabili wanafunzi katika taasisi za elimu ya juu.
Alisema katika kipindi cha mafunzo hayo, washiriki walipata nafasi ya kujifunza, kubadilishana uzoefu na kujadili changamoto mbalimbali wanazokutana nazo katika utekelezaji wa majukumu yao, pamoja na kupata mbinu mpya zitakazowawezesha kuboresha huduma wanazozitoa kwa wanafunzi.

"Nawapongeza viongozi wa TACOGA kwa ubunifu na maono yao ya kuhakikisha mafunzo haya yanafanyika kila mwaka. Bila uongozi imara, kuandaa mafunzo ya aina hii si jambo rahisi," alisema.
Aliongeza kuwa hatua hiyo inaonesha utambuzi wa umuhimu wa maendeleo endelevu ya kitaaluma kwa watendaji wanaohusika na huduma za wanafunzi pamoja na viongozi wa serikali za wanafunzi.
Badru alibainisha kuwa mada zilizowasilishwa zimegusa maeneo nyeti yanayoathiri ustawi na maendeleo ya wanafunzi, ikiwemo afya ya akili, maadili, matumizi ya teknolojia na uongozi bora.

Alisema dunia ya sasa inabadilika kwa kasi kutokana na maendeleo ya kijamii, kiuchumi na kiteknolojia, hali inayowafanya vijana kuwa miongoni mwa makundi yanayoathirika zaidi na mabadiliko hayo.

"Vijana wanakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo afya ya akili, matumizi mabaya ya teknolojia, matumizi ya dawa za kulevya na mmomonyoko wa maadili. Hivyo, kuna haja ya kuendelea kuwajengea uwezo na kuwapa mwongozo sahihi ili wawe raia wema na wazalendo," alisema.
Aidha, aliwakumbusha washiriki kuwa serikali na jamii kwa ujumla zinategemea sana mchango wa washauri na wanasihi katika kuwajenga wanafunzi.


Alisema wazazi na walezi wana matumaini makubwa kwa maafisa hao kwa kuwa vijana wengi wanaojiunga na vyuo vikuu bado wana umri mdogo na wanahitaji mwongozo, uangalizi na malezi ya karibu.
Kwa mujibu wake, kutokana na nafasi hiyo muhimu, TACOGA ina wajibu mkubwa wa kuchangia mageuzi ya maendeleo ya taifa kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050.

Alitoa wito kwa chama hicho kuwekeza zaidi katika mifumo ya kiteknolojia ili kuendana na mazingira ya sasa ya kidijitali. Alisema ni muhimu kuanzisha mifumo ya kimtandao na programu za simu zitakazowezesha wanafunzi kupata huduma za ushauri kwa haraka na kwa urahisi bila kuathiri muda wao wa masomo.

Pia aliwataka kuendelea kujenga uwezo wa wanachama wao kupitia mafunzo endelevu ya saikolojia, unasihi na mbinu mpya za utoaji wa huduma ili kuwawezesha washauri na wanasihi kutoa suluhisho stahiki na la kisasa kwa changamoto zinazowakabili wanafunzi.
Vilevile, alisisitiza umuhimu wa kuimarisha viashiria vya kupima matokeo ya kazi zinazofanywa na TACOGA kwa kuwekeza katika tafiti ndogo ndogo za kutathmini kama huduma zinazotolewa zinaleta matokeo chanya katika ufaulu wa wanafunzi na maendeleo yao ya kijamii na kitaaluma.

Mgeni rasmi huyo pia alisisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya ofisi za washauri wa wanafunzi na madawati ya jinsia pamoja na vitengo vya kuzuia ukatili wa kijinsia katika vyuo vikuu. Alisema kuna muunganiko mkubwa wa majukumu kati ya taasisi hizo, hivyo ushirikiano ukiimarishwa utasaidia kupunguza mzigo wa kazi na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wanafunzi.

Alisema maarifa na stadi zilizopatikana kupitia mafunzo hayo zinatarajiwa kuwafanya washiriki kuwa mabalozi wa mabadiliko katika taasisi zao na kuchangia kufikiwa kwa Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TACOGA, Sophia Nchimbi, alisema chama hicho kimeendelea kuandaa mafunzo hayo kwa lengo la kuwawezesha maafisa wa ofisi za washauri wa wanafunzi katika vyuo vikuu kutekeleza majukumu yao kwa weledi zaidi.

Alisema washiriki walipata mafunzo yaliyohusu nidhamu chanya, usimamizi wa tabia, unasihi, matumizi salama ya mitandao ya kijamii, afya ya akili, malezi ya wanafunzi, uongozi bora na usimamizi wa madawati ya jinsia katika vyuo vikuu.

"Mafunzo haya yanatusaidia kupata ufumbuzi wa changamoto mbalimbali tunazokutana nazo katika maeneo yetu ya kazi. Maarifa tunayopata yanatupa uwezo wa kuwahudumia wanafunzi kwa ufanisi zaidi," alisema Nchimbi.
Alisema mada kuhusu matumizi ya mitandao ya kijamii zimewawezesha washiriki kuelewa namna bora ya kuwaelekeza wanafunzi kutumia teknolojia kwa manufaa ya elimu badala ya matumizi yasiyofaa.

Nchimbi alisema pia washiriki walipata elimu kuhusu namna ya kusimamia madawati ya jinsia ili kuhakikisha wanafunzi wanaokumbana na changamoto mbalimbali wanapata msaada kwa wakati na kwa usahihi.

Aliongeza kuwa TACOGA imekuwa ikifanikiwa kuendesha mafunzo hayo kutokana na ushirikiano mkubwa wa wanachama na wadau mbalimbali wanaochangia maendeleo ya huduma za ushauri kwa wanafunzi.

Jumla ya washiriki 94 kutoka vyuo mbalimbali nchini walishiriki mafunzo hayo yaliyofanyika jijini Tanga.

Na Ashura Mohamed -Arusha 

Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) imepongeza uongozi wa Halmashauri ya Jiji la Arusha ukiongozwa na Mkurugenzi wa Jiji, Ndugu John L. Kayombo, pamoja na timu ya Menejimenti kwa usimamizi madhubuti wa miradi ya maendeleo na ushirikishwaji mzuri wa wananchi katika utekelezaji wake.

Pongezi hizo zimetolewa leo, Juni 6, 2026, wakati Kamati hiyo ilipotembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa Mradi wa Soko la Mrombo, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kutembelea na kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali ndani ya Jiji la Arusha.

Kamati hiyo imeeleza kuridhishwa na hatua za utekelezaji wa mradi huo pamoja na namna Halmashauri ilivyozingatia uwazi, usimamizi wa rasilimali za umma na ushirikishwaji wa wananchi, mambo ambayo yameendelea kuimarisha thamani na tija ya miradi ya maendeleo kwa jamii.

Aidha, wananchi waliofika katika eneo la mradi wakati wa ziara hiyo walitoa shukrani zao kwa Serikali kwa kutekeleza mradi huo mkubwa, wakieleza kuwa utakuwa chachu ya kukuza shughuli za biashara na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Jiji la Arusha na maeneo jirani.

Pamoja na pongezi hizo, wananchi hao waliomba kuboreshwa kwa miundombinu ya barabara zinazozunguka soko hilo mara baada ya kukamilika kwake. Akijibu ombi hilo, Mkurugenzi wa Jiji la Arusha, Ndugu John L. Kayombo, aliwahakikishia kuwa eneo lote linalozunguka Soko la Mrombo litaboreshwa kwa kujengwa barabara za lami ili kurahisisha usafiri na usafirishaji wa bidhaa.

Ziara ya Kamati ya LAAC ni sehemu ya jukumu lake la kusimamia matumizi sahihi ya fedha za umma na kuhakikisha miradi ya maendeleo inayotekelezwa inakidhi malengo yaliyokusudiwa na kutoa manufaa kwa wananchi.

Pongezi hizo zimetolewa leo, Juni 6, 2026, wakati Kamati hiyo ilipotembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa Mradi wa Soko la Mrombo, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kutembelea na kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali ndani ya Jiji la Arusha.

Kamati hiyo imeeleza kuridhishwa na hatua za utekelezaji wa mradi huo pamoja na namna Halmashauri ilivyozingatia uwazi, usimamizi wa rasilimali za umma na ushirikishwaji wa wananchi, mambo ambayo yameendelea kuimarisha thamani na tija ya miradi ya maendeleo kwa jamii.

Aidha, wananchi waliofika katika eneo la mradi wakati wa ziara hiyo walitoa shukrani zao kwa Serikali kwa kutekeleza mradi huo mkubwa, wakieleza kuwa utakuwa chachu ya kukuza shughuli za biashara na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Jiji la Arusha na maeneo jirani.

Pamoja na pongezi hizo, wananchi hao waliomba kuboreshwa kwa miundombinu ya barabara zinazozunguka soko hilo mara baada ya kukamilika kwake. Akijibu ombi hilo, Mkurugenzi wa Jiji la Arusha, Ndugu John L. Kayombo, aliwahakikishia kuwa eneo lote linalozunguka Soko la Mrombo litaboreshwa kwa kujengwa barabara za lami ili kurahisisha usafiri na usafirishaji wa bidhaa.

Ziara ya Kamati ya LAAC ni sehemu ya jukumu lake la kusimamia matumizi sahihi ya fedha za umma na kuhakikisha miradi ya maendeleo inayotekelezwa inakidhi malengo yaliyokusudiwa na kutoa manufaa kwa wananchi.












Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga, amesema dhana ya taka sifuri na urejeshaji bidhaa ni fursa muhimu ya kukuza sekta ya viwanda, kuongeza thamani ya malighafi na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa. 

Akizungumza katika kikao cha mawaziri kilichofanyika jijini Istanbul nchini Uturuki, Juni 5, 2026, kilichobeba mada ya Mageuzi ya Kijani ya Viwanda: Mtazamo wa taka sifuri na urejeshaji bidhaa, Kapinga amesema Tanzania inaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuimarisha sekta ya viwanda huku ikisisitiza matumizi bora ya rasilimali na uhifadhi wa mazingira.

Ameeleza kuwa dhana ya taka sifuri na urejeshaji bidhaa inatoa fursa kwa nchi zinazoendelea kupitia matumizi endelevu ya malighafi, kupunguza upotevu baada ya mavuno, kupunguza uzalishaji wa taka na kuongeza thamani ya bidhaa zinazotengenezwa viwandani. 

Kapinga amesema Serikali ya Tanzania imeendelea kuunganisha masuala ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi katika sera na mipango ya maendeleo ya viwanda kwa kuhamasisha matumizi ya nishati safi, ufanisi wa nishati na teknolojia rafiki kwa mazingira.


Aidha, amesisitiza kuwa mafanikio ya mageuzi ya kijani yanategemea uwekezaji wa kutosha, upatikanaji wa teknolojia za kisasa pamoja na ushirikiano madhubuti kati ya serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo. 

Amesema Tanzania itaendelea kushirikiana na jumuiya ya kimataifa kuendeleza viwanda vinavyoongeza thamani ya rasilimali, kudhibiti taka na kuvutia uwekezaji huku akiwakaribisha wafanyabiashara kuwekeza nchini kwa lengo la kujenga uchumi imara na shindani.

Mkutano huo umeandaliwa na Serikali ya Uturuki kupitia taasisi ya Zero Waste Foundation inayosimamiwa na Mwenza wa Rais wa Uturuki Bibi Emine ErdoÄŸan na umeleta pamoja washiriki zaidi ya 3,000 kutoka nchi zote duniani, pamoja na taasisi za kimataifa ikiwemo Benki ya Dunia, Umoja wa Mataifa, Benki ya Maendeleo ya Nchi za Kiarabu na Shirika la Maendeleo na Biashara la Umoja wa Mataifa (UNCTAD).

-Elimu bila malipo, Bima ya Afya kwa Wote ni ushindi

MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi CCM Taifa, Stephen Wasira, amesema ujamaa bado ni msingi mkuu unaoendesha sera na mipango ya maendeleo nchini.

Akizungumza na wanachama wa CCM mjini Moshi, leo Juni 6 2026, Wasira alisema alikana madai kuwa mfumo huo umepitwa na wakati.

"Wale wanaojidanganya hawaujui. Misingi inayoendesha nchi sasa ni ileile ya ujamaa. Tuanzie na elimu bila malipo, tuendelee na jitihada za kuanzisha Bima ya Afya kwa wote. Haya yote ni mafanikio ya ujamaa," alisema.

Wasira alitoa mfano wa Mkoa wa Kilimanjaro, akibainisha kuwa kama sio ujamaa, ardhi na mashamba ya kahawa yangekuwa yamenunuliwa na watu binafsi na wananchi wasingeweza kumiliki.

"Kama hapa Kilimanjaro tungekosa ujamaa, kahawa yote ingenunuliwa. Ni uongo kusema ingekuwa bado mikononi mwa wananchi," alieleza.

Pia, alizungumzia umuhimu wa uwekezaji wa sekta binafsi, akisema ni jambo la kawaida na la lazima kwa ukuaji wa uchumi wa nchi.

Akimnukuu Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Nyerere alisema: "Watu wote hawatakuwa na mapato sawa. Mkulima wa nyanya Kilimanjaro na mchimbaji wa gesi Lindi hawawezi kulingana. Hata wachimbaji madini nao hawalingani na wale wasiochimba."

Kwa mujibu wa Wasira, serikali inaleta haki kwa kuwatoza kodi wenye uwezo na kuwasaidia wasio na uwezo.

"Huwezi kujenga nchi bila mtaji. Wenye mtaji ni watu binafsi na kampuni. Kazi yetu ni kuwatoza kodi na kuwasaidia wanyonge," alisema.











 

 Na Mwandishi Wetu

MKURUGENZI Mtendaji wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB), Asangye Bangu ametoa onyo kali kwa watu wanaojihusisha na udanganyifu na uchakachuaji wa taarifa katika Mfumo wa Stakabadhi za Ghala na kusisitiza itaendelea kuchukua hatua ili kuhakikisha misingi ya uadilifu na uwazi inazingatiwa ipasavyo.

Bangu,ametoa onyo hilo baada ya kufanya kikao kikao kazi cha kujadili utekelezaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala katika Wilaya ya Malinyi mkoani Morogoro, kilichohudhuriwa na Mkuu wa Wilaya pamoja na viongozi na watendaji wa Halmashauri ya Wilaya hiyo.

Amesema mfumo huo unaendelea kufanya kazi kwa kuzingatia misingi ya uadilifu na uwazi, huku WRRB ikiendelea kushirikiana na mamlaka za mikoa, wilaya na halmashauri kusimamia utekelezaji wake.

“Moja ambalo nataka kuliweka wazi kwa Watanzania ni kwamba mfumo huu unafanya kazi kwa kuzingatia uadilifu. Kuna maeneo mengi mfumo unafanya vizuri, lakini tumeanza kuona baadhi ya watu wakiingiza taarifa zisizo sahihi kwenye mfumo kwa lengo la kujipatia fedha. Nataka nitoe onyo kali kwao kwamba tunasimamia mfumo huu kwa karibu na hatua stahiki zitachukuliwa,” amesema Bangu.

Ameeleza kuwa WRRB imeweka utaratibu wa kufanya uhakiki wa bidhaa zilizopo maghalani kabla ya kutolewa kwa katalogi za mauzo ili kuhakikisha wanunuzi wanapata taarifa sahihi kuhusu kiasi cha mazao yaliyopo.

Bangu pia amewahamasisha wakulima wa ufuta kuendelea kuuza mazao yao kupitia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala ili kupata masoko yenye ushindani na kuongeza kipato chao.

Amesema Serikali chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan imeendelea kuimarisha mazingira ya biashara ya mazao kupitia mfumo huo, jambo linalowezesha wakulima kunufaika zaidi na jasho lao.

“Wilaya ya Malinyi imeonyesha mafanikio makubwa katika utekelezaji wa mfumo huu. Miaka michache iliyopita kulikuwa na changamoto, lakini sasa tumeridhishwa na hatua zinazochukuliwa kuhakikisha wakulima wananufaika na mapato yao yanaongezeka,” amesema.

Katika hatua nyingine, WRRB imekabidhi msaada wa vifaa vya usafi na vyakula kwa Hospitali ya Wilaya ya Malinyi ikiwa ni sehemu ya shughuli zake za uwajibikaji kwa jamii.

Akikabidhi msaada huo katika Wodi ya Wazazi ya hospitali hiyo, Bangu amesema WRRB itaendelea kushirikiana na jamii sambamba na kutekeleza majukumu yake ya kusimamia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala nchini.

Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Wilaya ya Malinyi, Dk. Julius Nyasongo, aliyepokea msaada huo kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya, Wakili Sebastian Waryuba, ameishukuru WRRB kwa msaada huo akisema utasaidia kuboresha ustawi wa akina mama wanaopata huduma hospitalini hapo.

“Msaada huu utakuwa na mchango mkubwa kwa akina mama wanaopata huduma katika hospitali yetu. Tunawashukuru WRRB kwa kuendelea kushirikiana na sekta ya afya na jamii kwa ujumla,” amesema Dk. Nyasongo.

     
-Ni baada ya kuahidiwa kulipwa deni la sh. milioni 181


MKAZI WA CHUNYA, Bi Agnes Obeid Ole amelia machozi ya furaha mbele ya Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba baada ya kusikilizwa kero yake na kutolewa uamuzi kwamba mdaiwa atafutwe na amlipe sh. milioni 181 anazozidai.

“Kamanda wa Polisi mtafute huyo bwana. Mahakama ilikwishatoa hukumu na ikampa mama ushindi. Asakwe popote alipo, arudishe vifaa na arudishe fedha za huyu mama,” amesema Waziri Mkuu na kuamsha shangwe kwa wananchi waliokuwepo.

Waziri Mkuu ametoa agizo hilo leo (Jumamosi, Juni 6, 2026) wakati akizungumza na wananchi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye viwanja vya soko la Ifunda, wilayani Iringa, mkoani Iringa.

Akielezea kero yake, Bi. Agnes alisema kuwa kabla mumewe hajafariki, walikuwa wanachimba dhahabu kwenye mgodi wao huko Chunya lakini walimuomba rafiki yao, Bw. Lelevasi Fishulo mwenye mashine za kuchenjua washirikiane naye ili baadaye wagawane naye faida.

"Tulipata sh. milioni 362 lakini akasema amepata dharura na akaomba atulipe baadaye. Tukamkubalia. Mgao wetu ulikuwa sh. milioni 181 lakini siku ya kulipwa mume wangu akafariki, kwa hiyo nikaacha kufuatilia sababu ya maombolezo."

Bi. Agnes anasema baada ya mwaka mmoja kupita akamfuata kudai hela yake lakini hakumpa. "Nikaenda Serikali ya kijiji akaitwa kwa miezi mitatu hakutokea, nikaenda polisi akaitwa lakini ikapita miezi minne hakutokea ndipo nikaenda mahakamani kwa masuala ya mirathi," amesema.

Amesema alifungua kesi ya madai ya kudhulumiwa mali baada ya mumewe kufariki na mahakama ikampa haki ya kuwa msimamizi wa mirathi.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amemwagiza Kaimu Meneja TANROADS Mkoa wa Iringa, Mhandisi Hosea Machaka atafute fedha sh. milioni 47 za kumlipa Bi. Subira Mdoka ambaye anadai fidia ya shamba alilotoa kupisha ujenzi wa uwanja wa ndega wa Nduli.

Waziri Mkuu amechukua hatua hiyo baada ya kubaini kuwa TANROADS walifanya malipo ya fidia ya eneo lenye ekari 11 kwa Bw. Taaban ilhali eneo likiwa na mgogoro ambao ulikuwa umeshafikishwa mahakamani.

"Tafuteni akiba zenu mumlipe huyu Mama fedha yake kabla ya tarehe 30 Juni, 2026, kisha ninyi muendelee kumdai huyo bwana aliyewatapeli. Katibu Tawala wa Mkoa mtafuteni huyo bwana huko chuoni aelezwe haya maamuzi," amesema Waziri Mkuu.

Mhandisi Machaka alikiri kuwa walimlipa Bw. Taaban fedha hiyo wakati hukumu ya mahakama ilimpa ushindi Bi. Subira na wakawa wanamwambia asubiri fedha itakayorejeshwa na Bw. Taaban ndipo wamrejeshee.


-Walimu 35 walioshinda tuzo za ufundishaji kupatiwa viwanja

WALIMU nchini wamehimizwa kuendelea kufanya kazi kwa bidii, kujituma na kutumia mbinu bunifu za ufundishaji ili kuimarisha ubora wa elimu na kuchangia maendeleo ya taifa. Aidha, walimu 35 walioibuka washindi katika Shindano la Taifa la Stadi za Ufundishaji wameelekezwa kupatiwa viwanja karibu na maeneo yao ya kazi kama sehemu ya motisha.

Akizungumza Juni 6, 2026 jijini Dar es Salaam katika hafla ya utoaji wa zawadi kwa washindi wa shindano hilo kwa walimu wa elimu ya awali, msingi na sekondari, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Prof. Riziki Shemdoe, amesema walimu wana mchango mkubwa katika kuwalea na kuwaandaa wanafunzi kuwa wananchi wenye maarifa, stadi na maadili mema yanayohitajika katika jamii.

Prof. Shemdoe amesema Serikali itaendelea kuthamini mchango wa walimu kwa kuweka mazingira bora ya kazi pamoja na motisha mbalimbali zinazolenga kuongeza ufanisi katika ufundishaji na ujifunzaji.

Aidha, amewataka walimu kuendelea kutumia mbinu za kisasa na bunifu katika ufundishaji ili kuwajengea wanafunzi uwezo wa kufikiri kwa kina, kubuni na kukabiliana na changamoto za dunia ya sasa.

Amesema tuzo hizo zinalenga kuhamasisha ubora, uwajibikaji, ubunifu na kujituma katika kazi ya kufundisha, akisisitiza kuwa maendeleo ya taifa yanategemea kwa kiasi kikubwa ubora wa rasilimali watu inayozalishwa kupitia mfumo wa elimu.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo, Husna Sekiboko, amesema mafanikio katika sekta ya elimu yanahitaji ushiriki wa wadau wote, wakiwemo wazazi, walimu, wanafunzi pamoja na viongozi wa jamii.

Amesema maboresho yanayoendelea katika mifumo ya uongozi na utawala yanalenga kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma za elimu na kuimarisha matokeo ya ujifunzaji kwa wanafunzi.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Elimu Tanzania (TET), Dkt. Aneth Komba, amesema Shindano la Taifa la Stadi za Ufundishaji la mwaka 2026 ni la nne kwa walimu wa elimu ya awali na msingi, na la pili kwa walimu wa elimu ya sekondari, likihusisha halmashauri zote 184 za Tanzania Bara.

Amesema kwa upande wa elimu ya awali, shindano hilo limejikita katika kuimarisha umahiri wa ufundishaji wa stadi za kusoma, hususan matamshi ya sauti za herufi ambazo zimekuwa changamoto kwa baadhi ya wanafunzi katika kuzitamka na kuzitumia kwa usahihi wakati wa kuunda silabi na maneno.

“Lengo la shindano hili ni kusaidia kutatua changamoto za ufundishaji na ujifunzaji wa stadi za Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK) ili kuhakikisha wanafunzi wanazimudu stadi hizo muhimu wanapofikia Darasa la Tatu. Eneo hili la ushindani linaunga mkono maono ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha watoto wote wanasoma kwa ufasaha wanapofikia Darasa la Tatu,” amesema Dkt. Komba.

Ameeleza kuwa maandalizi ya shindano hilo yalihusisha uchambuzi wa matokeo ya wanafunzi kupitia taarifa za Baraza la Mitihani la Tanzania pamoja na maeneo mapya yaliyoingizwa katika mtaala, ili kubaini maeneo yanayohitaji kupewa kipaumbele.

Kwa mujibu wa Dkt. Komba, walimu walitakiwa kuandaa andalio la somo, kujirekodi wakifundisha kwa muda wa dakika 10 hadi 15, na kupakia video pamoja na andalio hilo katika mfumo wa kidijitali wa National Teaching Skills Competition System kwa ajili ya tathmini.

Jumla ya walimu 3,153 walijisajili katika mfumo huo, huku walimu 1,263 sawa na asilimia 40 wakifanikiwa kupakia video zao kwa ajili ya tathmini katika ngazi ya halmashauri.

Amesema tathmini ilifanyika katika ngazi tatu ambazo ni halmashauri, mkoa na taifa kwa kuzingatia vigezo mbalimbali, ikiwemo ubora wa maudhui, mtiririko wa somo, matumizi ya mbinu shirikishi, matumizi ya TEHAMA, matumizi ya zana za kufundishia, ukuzaji wa stadi za karne ya 21 pamoja na matumizi ya upimaji endelevu katika mchakato wa ufundishaji na ujifunzaji.

Katika mchujo wa shindano hilo, video 751 zilifanikiwa kuingia ngazi ya mkoa kutoka video 1,263 zilizotathminiwa katika ngazi ya halmashauri. Kati ya hizo, video 232 zilichaguliwa kuingia ngazi ya taifa.





Top News