Na Karama Kenyunko Michuzi Tv
WAZIRI katika Ofisi ya Rais anayeshughulikia Maendeleo ya Vijana, Joel Nanauka, amewataka vijana nchini kuzingatia elimu ya fedha akisema ni nyenzo muhimu ya kuwawezesha kiuchumi na kuwapa uwezo wa kushiriki kikamilifu katika agenda ya maendeleo ya taifa.

Nanauka ametoa wito huo leo Mei 5, 2026 wakati akizindua tawi jipya la Benki ya Ushirika (Coop Bank) jijini Dar es Salaam, ambalo ni tawi la sita la benki hiyo tangu kuanzishwa kwake.

Uzinduzi huo umeambatana na kusainiwa kwa makubaliano ya ushirikiano kati ya Coop Bank na Wizara ya Maendeleo ya Vijana yenye lengo la kuwajengea vijana maarifa ya kifedha na kuongeza ushiriki wao katika miradi mbalimbali ya maendeleo.

Akizungumza katika hafla hiyo, Nanauka amesema Coop Bank ni daraja muhimu linalowaunganisha vijana na fursa za kiuchumi pamoja na miradi ya maendeleo.
"Elimu ya fedha ni muhimu kwa vijana ikiwa wanataka kuwa huru kiuchumi na kuchangia kwa maana katika maendeleo ya taifa," amesema.

Ameongeza kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira rafiki yatakayowawezesha vijana kushiriki kikamilifu katika ukuaji wa uchumi wa nchi.
Aidha, aliwahimiza vijana kujiunga na mifumo rasmi ya kiuchumi na taasisi mbalimbali, akieleza kuwa hatua hiyo itawasaidia kukidhi vigezo vya kupata huduma za kifedha ikiwemo mikopo.

Mtendaji Mkuu wa Coop Bank, Godfrey Ng’urah, amesema tawi la Dar es Salaam ni la nne kufunguliwa mwaka huu. Alibainisha kuwa benki hiyo ilianza shughuli zake ikiwa na matawi matatu katika mikoa ya Mtwara, Kilimanjaro na Dodoma.

Ng’urah amesema benki hiyo inapanga kufungua jumla ya matawi 12 kabla ya mwisho wa mwaka kama sehemu ya mkakati wake wa kusogeza huduma katika vituo vikuu vya biashara nchini.

"Dhamira yetu ni kutoa suluhisho za kifedha kwa Watanzania kwa wakati na kwa kusogeza huduma za benki karibu zaidi na wananchi," amesema.

Ameongeza kuwa kupitia mfumo wa ushirika, benki hiyo inaamini kuwa ifikapo mwaka 2030 itakuwa imeongeza kwa kiasi kikubwa idadi ya wateja wake huku ikitumia teknolojia kuhamasisha maendeleo ya vijana na ujumuishaji wa kifedha.

Pia amesema Coop Bank iko tayari kushirikiana na taasisi za serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo katika juhudi za kuharakisha maendeleo ya taifa.
Naye, Mwenyekiti wa Bodi ya Coop Bank, Dkt.Joseph Witts, amesema benki hiyo imejizatiti kuunda fursa zitakazowasaidia vijana kuboresha hali zao za kiuchumi.
"Dar es Salaam inachangia kwa kiasi kikubwa uchumi wa taifa na ina fursa nyingi za uwekezaji na biashara," alisema.

"Kufunguliwa kwa tawi katika jiji hili kutafanya huduma za kifedha zipatikane kwa urahisi zaidi kwa wawekezaji, wafanyabiashara na wateja wetu wanaoongezeka."

Dkt. Witts alisema lengo kuu la benki hiyo ni kuweka maslahi ya wanachama wake mbele huku ikihakikqisha ukuaji endelevu na upanuzi wa shughuli zake.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Tume ya Maendeleo ya Ushirika, Abulmajid Nsekela, ambaye pia ni Mtendaji Mkuu wa CRDB Bank, amesema kuendelea kwa upanuzi wa Coop Bank ni mafanikio makubwa kwa harakati za ushirika nchini Tanzania.

"Ufunguzi wa tawi hili la Dar es Salaam ni hatua chanya na ni fursa ya kuhudumia vyama vingi vya ushirika vinavyofanya kazi katika jiji hili," alisema.

Pia amesisitiza umuhimu wa utawala bora, usimamizi madhubuti na matumizi ya teknolojia katika utoaji wa huduma bora za kifedha kwa Watanzania.
Kwa sasa, Coop Bank inaendesha matawi sita yaliyopo Dar es Salaam, Dodoma, Moshi, Tabora na matawi mawili mkoani Mtwara.





Wadau wa sekta ya ushirika mkoani Dodoma wamekutana katika Jukwaa la Maendeleo ya Ushirika Mkoa wa Dodoma kujadili utekelezaji wa maazimio yaliyopitishwa katika mikutano iliyopita, huku wakitathmini mafanikio yaliyopatikana na kuweka mikakati mipya ya kuimarisha vyama vya ushirika katika mkoa huo.

Akizungumza Juni 5, 2026, katika jukwaa hilo, Mrajisi Msaidizi wa Vyama vya Ushirika Mkoa wa Dodoma, Joseph Chintika, amesema jukwaa hilo ni la tano tangu kuanzishwa kwa utaratibu wa kuwakutanisha wadau wa ushirika kwa lengo la kujadili maendeleo, changamoto na fursa zilizopo katika sekta hiyo.

Amesema ushirika wenye mafanikio unategemea ushiriki wa wanachama wake na kuwataka washiriki kutumia nafasi hiyo kujadili kwa uwazi masuala yanayoikabili sekta hiyo ili kupata suluhisho la pamoja.

Chintika amesema serikali itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha vyama vya ushirika vinakuwa imara, vinazingatia sheria na kanuni zilizowekwa na vinatoa manufaa kwa wanachama wake pamoja na jamii kwa ujumla.

Katika mjadala uliofanyika, wadau mbalimbali wameeleza kuwa bado kuna changamoto zinazovikabili vyama vya ushirika, wamesema utekelezaji wa maazimio ya jukwaa hilo utasaidia kuimarisha utendaji wa vyama hivyo na kuongeza mchango wake katika maendeleo ya uchumi wa wananchi na Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake, mwakilishi kutoka Chuo Kikuu cha Ushirika Moshi (MOCU), Fredy Lyimo, amesema kujenga uaminifu miongoni mwa wanachama, viongozi na watendaji ni hatua muhimu katika kuhakikisha vyama vya ushirika vinaendelea kuwa imara na endelevu, ameongeza kuwa utekelezaji sahihi wa sera, sheria, kanuni na miongozo ya ushirika ni msingi wa mafanikio ya taasisi hizo.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Climb Up Limited, Emmanuel Ngallah, ameeleza umuhimu wa matumizi ya teknolojia, na mizani janja ya kidigitali, katika shughuli za ushirika,itaweza kusaidia kuongeza uwazi, kurahisisha utunzaji wa kumbukumbu na kuboresha utoaji wa huduma kwa wanachama.

Mkoa wa Dodoma una zaidi ya vyama vya ushirika 130 vinavyohudumia sekta mbalimbali za uzalishaji na biashara, wadau wa jukwaa hilo wameeleza matumaini yao kuwa kupitia majadiliano na utekelezaji wa maazimio yaliyofikiwa, vyama hivyo vitaendelea kuwa nguzo muhimu ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa mkoa huo.

Kaulimbiu ya Maendeleo ya Ushirika kwa mwaka 2026 inasema, “Ushirika kwa Dunia Yenye Amani; Linda Ushirika, Chagua Uadilifu,” ikisisitiza umuhimu wa maadili na uwajibikaji katika kuimarisha harakati za ushirika nchini.


Taasisi ya INADES Formation Tanzania imeadhimisha Siku ya Mazingira Duniani kwa kupanda miti 200 ya kivuli na matunda katika Shule ya Sekondari Kisima cha Ndege iliyopo Wilaya ya Bahi mkoani Dodoma.

Zoezi hilo ni sehemu ya mwendelezo wa kampeni ya “Panda Mti Tuilinde Kesho” iliyozinduliwa Januari 2026, yenye lengo la kuchangia juhudi za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na kuimarisha utunzaji wa mazingira.

Akizungumza baada ya shughuli ya upandaji miti iliyofanyika Juni 5, 2026, Mwakilishi wa INADES Formation Tanzania, Paul Ephras Chugu, amesema taasisi hiyo imefanikiwa kupanda miti zaidi ya 15,000 katika vijiji vinne vya Wilaya ya Bahi tangu kuanza kwa kampeni hiyo.

Kwa upande wake, Afisa Mazingira wa Halmashauri ya Wilaya ya Bahi, Joyce Anania Jackson, ameipongeza INADES Formation Tanzania kwa ushirikiano mzuri unaoendelea kati ya taasisi hiyo na halmashauri katika kutekeleza shughuli za uhifadhi wa mazingira.

Naye Mkuu wa Shule ya Sekondari Kisima cha Ndege,  Mwalimu wa Mazingira na Mwenyekiti wa Klabu ya Mazingira wa shule hiyo, wamepongeza juhudi za taasisi hiyo kwa kuendelea kutoa elimu na kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa utunzaji wa mazingira.

Maadhimisho hayo ya Siku ya Mazingira Duniani yaliambatana na bonanza la michezo lililowakutanisha wanafunzi wa shule hiyo, wanafunzi kutoka shule jirani pamoja na wananchi wa vijiji vya jirani, kwa lengo la kutoa elimu kuhusu uhifadhi wa mazingira na kuhamasisha ushiriki wa jamii katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.







WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kusimamia utoaji wa haki kwa wananchi na kuimarisha uwajibikaji kwa watumishi wa umma ili kuhakikisha huduma za Serikali zinatolewa kwa ufanisi, kwa wakati na kwa kuzingatia maslahi ya wananchi.

Amesema hayo leo Ijumaa, Juni 5, 2026 alipokuwa akizungumza na kusikiliza kero za wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa katika Jimbo la Isimani mkoani Iringa katika viwanja vya Isimani tarafani.

Dkt. Mwigulu amesema haki za wananchi hazipaswi kucheleweshwa wala kunyimwa kwa sababu yoyote na kusisitiza kuwa kila anayestahili haki yake anapaswa kuipata kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizowekwa.

“Haki si hisani. Tunataka anayestahili haki apewe haki yake. Serikali haitavumilia vitendo vya kupora au kuchelewesha haki za wananchi kwa sababu yoyote ile,” amesema.

Aidha, Waziri Mkuu amesema watumishi wa umma wanapaswa kutambua kuwa nafasi walizonazo ni dhamana ya kuwatumikia wananchi na kwamba huduma zinazoweza kutolewa kwa siku hiyo zinapaswa kutolewa bila kuwazungusha wananchi.

“Linaloweza kufanyika leo lifanyike leo. Wananchi wanapofika katika ofisi za umma wanapaswa kuhudumiwa kwa heshima, haraka na kwa ufanisi,” amesema.

Pia amesema Serikali itaendelea kuchukua hatua kali dhidi ya watumishi watakaobainika kushindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo, hususan wale wanaokwaza utoaji wa huduma na matumizi sahihi ya rasilimali za umma.

Waziri Mkuu amesema uwajibikaji, uadilifu na utoaji wa huduma bora ni msingi muhimu wa kujenga imani ya wananchi kwa Serikali na kuhakikisha maendeleo yanawafikia wananchi wote.

Kadhalika, amewahakikishia wananchi wa Isimani kuwa Serikali itaendelea kutekeleza ahadi zilizotolewa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na miradi ya maendeleo iliyopo kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi kwa lengo la kuboresha maisha ya wananchi.









Na Jawadu Kinyobwa - Dsm

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete amewataka Wanafunzi wa sheria kujenga taaluma zao katika misingi ya nidhamu, ubunifu na uzalendo ili waweze kufanikiwa katika soko la ajira la kimataifa linalozidi kuwa na ushindani.

Akizungumza leo Juni 5, 2026 katika hafla ya Siku ya Kazi na Taaluma ya Shule ya Sheria ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, amesema mafanikio ya kitaaluma hayawezi kupatikana bila kuzingatia maadili hayo matatu muhimu.

Akifafanua kuhusu nidhamu, amesema ubora si jambo la muda mfupi bali ni tabia inayojengwa kwa kujifunza kwa bidii, kutunza muda, kuwa na hamu ya kujifunza mambo mapya na kuzingatia maadili ya taaluma. 

Amefafanua kuwa, nidhamu inayojengwa kupitia mahakama za mfano, kazi za kitaaluma na shughuli za msaada wa kisheria ndiyo msingi wa kukabiliana na changamoto za taaluma katika ngazi za kitaifa na kimataifa.

Aidha, kuhusu ubunifu, Waziri huyo amesema maendeleo ya teknolojia yamebadili kwa kiasi kikubwa namna taaluma ya sheria inavyotekelezwa duniani. Ametaja matumizi ya Akili Mnemba, mifumo ya kidijitali ya usajili na teknolojia za kisheria kuwa miongoni mwa mabadiliko yanayounda upya mazingira ya kazi za sheria. 

Katika hatua nyingine, amesisitiza umuhimu wa uzalendo, akieleza kuwa wao ni walinzi wa utawala wa sheria na utawala bora hivyo wanapopata fursa ya kufanya kazi  katika taasisi za kimataifa au kampuni kubwa nje ya nchi, wanapaswa kutumia maarifa na uwezo wao kuisaidia Tanzania kutambulika vyema nje ya nchi.

Sambamba na hayo, Amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuimarisha sekta ya sheria na haki kupitia mageuzi ya mfumo wa haki, matumizi ya teknolojia, uwekezaji katika miundombinu ya utoaji haki na kuhamasisha mifumo mbadala ya utatuzi wa migogoro.

Awali, akizungumzia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mhe. Ridhiwani amesema sekta ya sheria ni nguzo muhimu katika kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii kupitia mchango wa wataalamu wa sheria katika kulinda maslahi ya taifa, kuimarisha utawala wa sheria na kusaidia mageuzi ya kidijitali.

Na Beda Msimbe,TBN, Moscow

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk Samia Suluhu Hassan amesema wakati umefika kwa Tanzania na Urusi kutekeleza makubaliano na kuacha maneno katika kufanikisha makubaliano yanayokuza biashara na uwekezaji.

Amesema kwamba uwekezaji Tanzania unalipa hasa katika mikakatik ambayo imelenga kutekeleza Dira ya maendeleo ya 2050.

Alisema kwamba milango ya Tanzania ipo wazi kuona kwamba makubaliano ya ujenzi wa viwanda vya dawa, viua dud una uwekezaji kwimngine unfanyuiwa kazi kwa manjufaa ya pande zote mbili.

Alisema ikiwa sehemu ya kurahisha utekelezaji wa mikataba ya uwekezaji kuanzia Julai 2 mwaka huu Shirika la Ndege (ATCL) litaanza safari za moja kwa moja kutoka Dar es Salaam, Moscow na Zanzibar.

Aidha ni matarajio ya Rais Samia kwamba Shirika la Ndege la Urusi la Azur pia litanza safari hizo.

Akizungumza na wafanyabiashara juu ya nafasi ya wananchi wa pande zote mbili kunufaika na uhusiano huo, Rais Samia alizungumzia kuhusu uwekezaji wa Urusi nchini Tanzania na kuwaita wafanyabuashara na wawekezaji katika nishati, madini, dawa za binadamu, viwatilifu na kilimo na kusema mabadiliko makubwa yanatakiwa kufanywa ili kupunguza urari wa biashara.

Alisema kwamba ujazo wa sasa biashara hauakisi ukweli kuwa kuna nafasi kubwa ya kuwapo kwa maendeleo ya ushirikiano hasa katika n yajna ambazo ni za kimkakati zinazolenga kuihudumia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050.

Naye Waziri wa Maendeleo ya Kiuchumi wa Urusi, Maxim Reshetnikov amesema kwamba amefurahishwa na juhudi za kuifungua Tanzania zinazofanywa na Rais Samia Suluhu Hassan.

Alisema juhudi hizo zinazaa matunda na kwamba Urusi ipo tayari kushirikiana na Tanzania katika miradi yake ya kimkakati.

Anasema taifa hilo litaendelea kufungua fursa mbalimbali kwa kuwekeza nchini Tanzania katika kilimo na teknolojia na viwanda

“Tanzania ni lango la mashariki ya kati tupo tayari kuwapatia teknolojia na utaalamu wetu na tupo tayari kushiriki katika kuanzisha viwanda mbalimbali vya dawa na mbolea” alisisitiza waziri huyo akishukuru kwa namna ambavyo wafanyabiashara wa Tanzania walivyofika kwa wingi baada ya mkutano wa Arusha, kushiriki katika ukamilishaji wa mambo mbalimbali.

Aidha mmoja wa wafanyabiashara wa Kitanzania akizungumza baada ya kukamilika kwa kongamano hilo, Dhruv Jog, amesema kualikwa kwa wafanyabiashara katika safari ya Rais na kushiriki kongamano hilo inaonesha ni kwa namna gani sekta binafsi inathaminiwa katika kubadili maisha ya Watanzania.

Alisema kitendo hicho kinasaidia kuifungua jumuiya ya sekta binafsi katika daraja jingine. Alisema kufanikiwa kufungua soko la Urusi kutawezesha watanzania kufanya biashara na nchi takribani 15 zinazofanya ukanda wa Urusi hivyo kuleta kipato zaidi.

Katika ziara hii ya kihistoria ikifanywa kwa mara ya pili katika historia ya uhusiano wa Tanzania na Urusi, ya kwanza ilikuwa ni miaka ya 1960 iliyofanywa na baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere, Rais Samia anaendeleza kampeni kubwa ya kuhakikisha Tanzania inanufaika pia kiuchumi na uhusiano mzuri na mataifa mbalimbali.

Akiwa hapa Rais Samia alifanya mazungumzo na Rais Vladmir Putin katika lengo la kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia, kisiasa, kiuchumi na kihistoria baina ya Tanzania na Urusi

Pia Rais Samia ameiweka Tanzania katika ramani ya uwekezaji kwa hotuba yake aliyoitoa katika mkutano mkubwa wa uwekezaji jijini St Petersburg.








Spika Zungu Aonya Matumizi ya Lugha za Kudhalilisha Bungeni, Kauli ya Mbunge Lucy Mayenga Kufutwa HansadNa Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mussa Azan Zungu, amesisitiza umuhimu wa wabunge kuzingatia kanuni, sheria na maadili ya Bunge kwa kuepuka matumizi ya lugha za matusi au kauli zinazoweza kuwadhalilisha wabunge wenzao wakati wa mijadala ya kibunge.

Akiongoza shughuli za Bunge leo Spika Zungu ameeleza kuwa kauli iliyotolewa na Mbunge Lucy Mayenga ya kusema kuwa “mbunge Sigrada Mligo (CHAUMA) hajitambui” ni kauli ya kuudhi na yenye kudhalilisha mbunge mwingine, jambo ambalo halikubaliki ndani ya chombo hicho cha juu cha kutunga sheria.

Amesema kuwa matumizi ya lugha zisizofaa yanakiuka kanuni za Bunge na yanaweza kuathiri hadhi na heshima ya mijadala ya kitaifa inayofanyika ndani ya ukumbi wa Bunge.

Kutokana na tukio hilo, Spika Zungu alitoa onyo kali kwa wabunge wote, akiwataka kujiepusha na kauli zinazoweza kuleta mvutano au kudhalilisha wenzao, huku akisisitiza kuwa nidhamu na heshima ni msingi muhimu wa uendeshaji wa shughuli za kibunge.

Aidha, aliamuru kauli hiyo iliyotolewa na Mbunge Lucy Mayenga iondolewe kwenye hansadi rasmi za Bunge kwa kuwa imeonekana kwenda kinyume na taratibu na maadili ya chombo hicho.

Katika hatua nyingine, Spika Zungu aliwataka wabunge kuendelea kuzingatia sheria, kanuni na maadili ya kibunge ili kulinda heshima ya Bunge na kuhakikisha mijadala inafanyika kwa ustaarabu na kwa maslahi ya taifa.

Awali, Spika huyo alimwapisha rasmi Mbunge mpya wa Jimbo la Isimani, Emanuela Mtafikikolo Kaganda, ambaye amechukua nafasi iliyoachwa wazi kufuatia kifo cha aliyekuwa Mbunge wa jimbo hilo, William Lukuvi.


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ametoa wito wa kutumia Maadhimsho ya Siku ya Mazingira Duniani kukumbuka wajibu wa kuunganisha nguvu katika jitihada za kuhifadhi mazingira, na kuhakikisha matumizi adili ya rasilimali nyingi ambazo Tanzania imejaaliwa kuwa nazo.

Makamu wa Rais ametoa wito huo, alipomwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani, ambayo Kitaifa yamefanyika katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete mkoani Dodoma.

Amesema baadhi ya mambo muhimu ya kuzingatia katika uhifadhi wa mazingira ni pamoja na kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu masuala ya mazingira na kuimarisha mfumo wa usimamizi wa taka hususan katika Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa dhana ya uchumi rejeshi, kwa kuwa maeneo mengi bado hali ya usafi haridhishi.

Makamu wa Rais ameongeza kwamba, ni vema kuendelea kubadili mtazamo ili kuziona taka kama fursa ya kiuchumi na kuzitumia kutengeneza bidhaa mbalimbali kama vile mbolea, chakula cha mifugo na bidhaa nyinginezo. Hali kadhalika, kuendelea kutekeleza Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia ambapo hadi sasa, matumizi hayo yameendelea kuimarika kutoka 6.9% mwaka 2021 hadi kufikia 28.6% mwaka 2025.

Aidha, Makamu wa Rais amehimiza kuongezwa kwa jitihada za uhifadhi na utunzaji wa mazingira ambapo ameagiza Mamlaka zinazotoa vibali vya ujenzi kuweka sharti na kusimamia ili kila kibali cha ujenzi kinachotolewa kinaambatana na agizo la kupanda miti isiyopungua mitano pamoja na kuzielekeza Mamlaka za Serikali za Mitaa hususan Manispaa na Majiji kuazisha Bustani za kijani na kuhakikisha zinatunzwa ipasavyo.

Pia Makamu wa Rais ameagiza Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania kuhakikisha uwepo wa miche ya miti ya kutosha ili kurahisisha na kuwezesha zoezi la upandaji miti nchini, Mamlaka husika kuimarisha udhibiti wa uharibifu wa maeneo yote yanayopandwa miti pamoja na kuiagiza Ofisi ya Makamu wa Rais kupitia kituo cha Taifa cha kuratibu kaboni kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), kubainisha misitu inayofaa na kuisajili katika biashara ya kaboni.

Vilevile, Makamu wa Rais ametoa rai kwa Taasisi za utafiti kufanya tafiti kuhusu mimea au viumbe vamizi ambavyo vinazidi kuongezeka na kuathiri mifugo na mimea mingine katika maeneo mbalimbali nchini. Pia ameagiza Mamlaka za Serikali za Mitaa kuimarisha mifumo ya usimamizi wa taka hususan kuanzisha vituo vya kuchakata taka ili kupunguza kiasi cha taka katika madampo na kuchagiza urejelezaji.

Makamu wa Rais ametoa wito kwa kila mwananchi kuwajibika kuhakikisha kwamba suala la utunzaji na usafi wa mazingira, ikiwemo udhibiti wa taka linapewa kipaumbele. Amesema ni vema kutambua suala la ulinzi na uhifadhi wa mazingira halina mbadala, kwa kuwa mazingira ndiyo uhai na uchumi.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhandisi Hamad Masauni, amesema Uzinduzi wa Programu ya Mageuzi ya Kimkakati ya Mazingira Endelevu Tanzania, itakayotekelezwa kwa kipindi cha miaka mitano (2026 – 2030), imelenga kuchochea matokeo makubwa ya haraka katika kurejesha uoto wa asili, kuimarisha ustawi wa mfumo wa ikolojia pamoja na kutoa huduma za kiikolojia ambazo ni msingi muhimu wa uzalishaji katika sekta mbalimbali za uchumi.

Amesema hatua hizo zitaweza kuchangia katika kufanikisha malengo ya Dira 2050 ambayo inalenga kuifanya nchi kuwa na ustawi wa mazingira na ustamilivu mkubwa wa mabadiliko ya tabianchi. Ameongeza kwamba Programu hiyo, inalenga kuhamasisha upandaji wa miti bilioni mbili kila mwaka, kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia, kuimarisha usimamizi wa taka, kukuza biashara ya kaboni pamoja na kuongeza ushiriki wa wananchi hususani wanawake na vijana katika uchumi wa kijani.

Maadhimisho hayo, yaliobebwa na kauli mbiu isemayo, “Dira 2050: Tuwajibike Kukijanisha Tanzania” yamehudhuriwa na wadau mbalimbali wa mazingira wa Kitaifa na Kimataifa, Viongozi mbalimbali, Wanafunzi na Wananchi.








 Na Mwandishi Wetu

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) inaandaa mapendekezo ya  kufanya maboresho ya  Kanuni za Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, ili kuwezesha wahitimu wa taaluma za Habari, Uhusiano na Mawasiliano kwa Umma kupata ithibati bila sharti la kuwasilisha barua ya mwajiri.

Hayo yamesemwa leo tarehe 05 Juni, 2026 na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, wakati akiwasilisha mada kuhusu “Uhuru wa Vyombo vya Habari katika Enzi ya Kidijiti: Wajibu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari” kwenye Kongamano la Uhuru wa Vyombo vya Habari lililoandaliwa na Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) kupitia Idara ya Sanaa na Taaluma za Habari.

Wakili Kipangula amesema maboresho hayo yanalenga kupanua wigo wa wanufaika wa mfumo wa ithibati kwa kuwajumuisha wahitimu wa taaluma hizo mara tu wanapomaliza masomo yao, hatua itakayowawezesha kuwa tayari kuingia katika soko la ajira au kujihusisha na shughuli za kitaaluma zinazohitaji ithibati wakati wowote.

Amesema kwa sasa Kanuni  za Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, zinamtaka mwombaji wa ithibati kuwasilisha nyaraka za kitaaluma pamoja na barua ya utambulisho kutoka kwa mwajiri au chombo cha habari, taasisi au jukwaa analopeleka kazi zake za kitaaluma.

Kwa mujibu wa Kipangula, mapitio ya kanuni hizo yatawezesha kuondoa changamoto zinazowakabili baadhi ya wahitimu wapya ambao wanakidhi sifa za kitaaluma lakini bado hawajapata waajiri au taasisi za kuwapatia barua za utambulisho zinazohitajika katika mchakato wa maombi ya ithibati.

Awali kabla ya kumkaribisha Wakili Kipangula kutoa wasilisho Mkuu wa Idara ya Sanaa na Taaluma za Habari katika Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Dkt. Deograsia Ndunguru, ameikaribisha Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) kuendelea kuimarisha ushirikiano na Chuo hicho katika maeneo mbalimbali, ikiwemo maboresho ya mitaala ya uandishi wa habari ili kuendana na mabadiliko ya teknolojia na mahitaji ya sekta ya habari.

Shule ya Royal Family English Medium Primary School imeendelea kujijengea sifa kubwa baada ya kuibuka kinara kwa kushika nafasi ya kwanza katika Manispaa ya Geita kati ya shule 91 katika mtihani wa Moko ya Kanda ya Ziwa.

Shule hiyo yenye wanafunzi 77 wa darasa la saba walioshiriki mtihani huo wameonyesha kiwango cha juu cha ufaulu ambapo wanafunzi 76 wamepata wastani wa A na mwanafunzi mmoja pekee akipata wastani wa B.

Akizungumza baada ya kutangazwa kwa matokeo hayo Mkurugenzi wa shule Mhandisi Lazaro Philipo amesema mafanikio hayo ni matokeo ya ushirikiano mkubwa kati ya walimu, wazazi na wanafunzi.

Ameishukuru jamii kwa kuendelea kuiamini shule hiyo na kuahidi kuongeza juhudi zaidi ili kuifanya Royal Family kuwa kitovu cha elimu bora na maadili mema nchini.


NA MWANDISHI WETU, DODOMA


Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) na Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa (MCC), Mary Chatanda amesema mageuzi makubwa ya kimaendeleo yaliyofanywa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan yamekuwa chachu ya vyuo vikuu vya ndani na nje ya Tanzania kumtunuku Shahada mbalimbali za Heshima za Uzamivu.

Chatanda ametoa kauli hiyo Juni 5, 2026, Jijini Dodoma ikiwa ni siku moja imepita tangu Chuo Kikuu cha Urafiki wa Watu wa Urusi (RADN University) kumtunuku Shahada ya Udaktari wa Heshima (Honoris Causa), Jijini Moscow, Urusi.

"Unajua utendajikazi mzuri wa Rais wetu Dk. Samia unaonekana duniani kote, na wengi wanaridhishwa na juhudi kubwa zinazofanywa ana serikali katika kuchochea maendeleo ya nchi. Rais amefanya mageuzi makubwa ya kimaendeleo, na ndiyo maana wenzetu wa Urusi wamemtunuku Shahada ya Udaktari wa Heshima," amesema Chatanda.

Sambamba na hilo, Chatanda amesema katika kila sekta, kuna mabadiliko chanya mengi ambayo yamefanyika ndani ya muda mfupi, ndiyo maana hata mataifa mengine yanatambua kazi nzuri zinazofanyika nchini.

Juni 4, 2026, Chuo Kikuu cha RADN kilimtunuku Rais Dk. Samia Shahada ya Udaktari wa Heshima ikiwa ni njia ya kutambua mchango wake katika mageuzi ya sekta ya elimu, kuimarisha hadhi ya Tanzania kimataifa ikiwemo sekta ya utalii.

Baada ya kutunukiwa Shahada hiyo, Rais Dk. Samia amesema mafanikio hayo si yake pekee yake bali ni juhudi za pamoja kama nchi.

"Shahada hii haihusu mafanikio yangu binafsi, bali ni utambuzi wa mchango wa Watanzania wote katika maendeleo ya Taifa na ushirikiano wa kimataifa. Napokea kwa upole, kama Rais wa Tanzania, mtoto wa Afrika na rafiki wa Russia. Siipokei kwa ajili yangu, bali kwa ajili ya Watanzania," amesisitiza Rais Dk. Samia.

Rais Dk. Samia yupo nchini Urusi kwa ziara ya kikazi, ikiwa ni juhudi za kuimarisha diplomasia ya uchumi na mataifa mengine ili kukuza maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii nchini.



Top News