Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam Rais Mstaafu Dkt Jakaya Mrisho Kikwete akiwa na Mkuu wa Harvard Kennedy School, Prof. Jeremy M. Weinstein baada ya mazungumzo yao huko Marekani)

CHUO Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kimeingia katika mazungumzo ya ushirikiano wa kimkakati na Chuo Kikuu cha Harvard, Marekani, yakilenga kuimarisha matumizi ya Akili Mnemba (AI) katika elimu, utafiti na uchambuzi wa taarifa.

Mazungumzo hayo yalianzishwa na Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, alipokuwa katika ziara ya kikazi nchini Marekani.

Ushirikiano huo unalenga kujenga uwezo wa kutumia AI kwa ufanisi katika kufundishia, kuongeza kasi ya tafiti, na kurahisisha uchakataji wa taarifa nyingi kwa wakati mfupi, eneo ambalo linazidi kuwa muhimu katika vyuo vikuu duniani.

Katika kipindi ambacho taasisi za elimu ya juu zinakabiliana na changamoto na fursa zinazotokana na AI, hatua ya UDSM kuingia katika mazungumzo na Harvard inaonekana kama mkakati wa mapema wa kuhakikisha Tanzania haiwi nyuma katika mapinduzi ya teknolojia.

Akizungumza katika kikao hicho, Dkt. Kikwete alisisitiza umuhimu wa matumizi sahihi na yenye uwajibikaji ya AI, akibainisha kuwa teknolojia hiyo inaweza kuwa nyenzo muhimu ya kuboresha ubora wa elimu na utafiti iwapo itasimamiwa vyema.

Kwa upande wa Harvard, majadiliano yalihusisha viongozi na wataalamu waandamizi, akiwemo Mkuu wa Harvard Kennedy School, Prof. Jeremy M. Weinstein, pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Maendeleo ya Kimataifa (CID), Dkt. Fatema Sumar.

Aidha, timu ya wataalamu wa AI kutoka Harvard ilishiriki majadiliano hayo, wakiongozwa na Prof. Sharad Goel, akishirikiana na Dkt. Dan Levy na Dkt. Teddy Svoronos—wote wakiwa na uzoefu mkubwa katika matumizi ya AI katika sera za umma na uchambuzi wa data.

Ushirikiano huu unatarajiwa kufungua ukurasa mpya katika sekta ya elimu ya juu nchini, kwa kuunganisha utaalamu wa ndani na uzoefu wa kimataifa katika matumizi ya teknolojia ya kisasa.

-Bilioni 3.2 kutumika kukamilisha miradi Ludewa, Njombe

-Wananchi, taasisi za kijamii kuanza kunufaika na nishati ya REA

-Sekta za uvuvi, afya na elimu kupata mapinduzi makubwa


Ludewa, Njombe📍

Matumaini ya ukuaji wa uchumi na uboreshaji wa huduma za kijamii yameongezeka kwa wakazi wa mwambao wa Ziwa Nyasa, wilayani Ludewa, kufuatia hatua ya Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kufikisha miradi ya umeme kwenye vitongoji vya eneo hilo.

Katika ziara ya Bodi ya Nishati Vijijini (REB) iliyolenga kukagua maendeleo ya miradi hiyo mkoani Njombe, imebainika kuwa kiasi cha Shilingi Bilioni 3.2 kimetengwa kwa ajili ya kukamilisha miradi ya kusambaza nishati hiyo katika wilaya ya Ludewa.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo katika Shule ya Msingi Lumbila, Mwalimu Mkuu Msaidizi, John Mwasoso, amesema ujio wa umeme ni ukombozi katika mazingira ya kufundishia na kujifunzia. Alibainisha kuwa tayari wameanza maandalizi ya awali kwa kufanya mifumo ya nyaya (wiring) kwenye baadhi ya vyumba vya madarasa na nyumba za walimu.

Kwa upande wao, wananchi wa kitongoji cha mabatini wameonyesha shauku ya kutumia nishati hiyo kuchochea uchumi wao, hususan katika sekta ya uvuvi. Bwana Augustino Madesu, mkazi wa eneo hilo, alisema umeme utawasaidia kuhifadhi samaki kwa kutumia majokofu (friza), jambo litakalowaepushia hasara ya kuuza samaki kwa bei ya kutupa pindi wanapovua kwa wingi.

Naye Mganga Mfawidhi wa zahanati ya Nkanda, Timotheo Nkwabi, alieleza kuwa umeme utamaliza changamoto ya kutoa huduma za afya gizani wakati wa usiku na kuimarisha mifumo ya kidigitali ya utunzaji wa kumbukumbu za wagonjwa na dawa.

Mkurugenzi wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Mhandisi, Ahmed Chinemba, amewahakikishia wananchi kuwa serikali imeweka kipaumbele kwenye taasisi za umma kama shule, zahanati na miradi ya maji ili kuhakikisha wananchi wananufaika kwa haraka.

“Tunawahamasisha wananchi kujiandaa kwa kufanya ‘wiring’ kwenye majengo yao ili waweze kuupokea umeme mara tu unapofika. Lengo ni kuona nishati hii inabadilisha maisha ya mtanzania wa vijijini,” alisema Mhandisi, Chinemba.

Naye Kaimu Meneja Msimamizi wa Miradi REA, Mhandisi Deogratius Nagu, aliongeza kuwa kutokana na ongezeko la mahitaji, Bodi ya Nishati Vijijini (REB) imeelekeza kuongezwa kwa idadi ya wanufaika ili kuhakikisha kaya nyingi zaidi zinapata nishati hiyo kabla ya mradi kukamilika rasmi.

Kukamilika kwa mradi huu kunatarajiwa kufungua fursa mpya za ajira kwa vijana kupitia vijiwanda vidogo, saluni, na biashara nyinginezo zinazotegemea nishati ya umeme, huku kukiimarisha usalama na ustawi wa jamii katika mwambao wa Ziwa Nyasa.





Na Mwandishi Wetu

KAMPUNI ya Oryx Gas Tanzania imesema mkakati wake ni kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia huku pia ikisisitiza umuhimu wa elimu ya mara kwa mara kwa watumiaji ili wawe na uelewa namna bora ya kutumia nishati safi ya kupikia

Hivyo katika kufanikisha mkakati huo Oryx Gas imesema imeamua kuanzisha maduka maalum yatakayotumika kuhamasisha wananchi kutumia nishati safi kwa kusogeza huduma hiyo karibu lakini wakati huo huo maduka hayo yatatumika kutoa elimu ya matumizi bora na salama ya nishati safi.

Akizungumza leo Aprili 30,2026 wakati wa ufunguzi wa duka maalum la kuuza mitungi ya Gesi ya Oryx lililopo eneo la Banana jijini Dar es Salaam Menaja Masoko na Mauzo Shaban Fundi amesema wanatambua juhudi za serikali katika kuhimiza nishati safi.

“Sisi Oryx Gas ni vinara wa nishati safi ya kupikia hivyo tumeunganisha nguvu zetu kwa kuunga mkono jitihada za Serikali kuhakikisha matumizi ya nishati safi ya kupikia yanafika kwa wananchi wote.Tunatambua namna gani Serikali inatamani ifikapo mwaka 2030 basi asilimia 80 ya Watanzania iwe inatumia nishati safi ya kupikia 

“Kwahiyo ufunguzi wa maduka haya maalum ni muendelezo wa muunganiko wetu kuunga mkono juhudi za Serikali na wananchi kwa ujumla kwamba nishati safi sio anasa bali ni lazıma kwamba watu wapate nishati safi ya kupikia na sisi kama Oryx tumeendelea kuboresha miundombinu ya kuhifadhi ,kupokea pamoja na usambazaji lengo ni kuona huduma inafika kwa jamii.”

Kuhusu elimu ya namna bora ya kutumia nishati safi ya kupikia amesema ni jambo la msingi wananchi kujengewa uelewa kuhusu matumizi ya nishati hiyo kwani usipojua namna ya kuitumia vizuri unaweza kuona ni gharama au inakwisha mapema kumbe anayetumia hajui jinsi ya kutumia hasa kufungua mtungi au jinsi ya kuufunga.

“Kwahiyo wananchi wakifika katika maduka yetu watapata elimu ya namna gani wanaweza kutumia nishati safi ya kupikia mitingi yetu.Mbali ya kupata elimu hiyo Oryx Gas tumekuja na utaratibu wa kupeleka huduma kwa wananchi kwani ukishanunua mtu hutaubeba bali utaacha namba ya simu na sisi tutakuletea mpaka ulipo kwa gharama zetu.

“Hivyo ili kuhakikisha wananchi wanapata nishati safi kwa wakati tunaendelea na kufunga maduka haya maalum ambako kwa nchi nzima yapo 1000 na tunaendelea kufungua mengine likiwemo hili la Banana kwa NASSCO na wiki iliyopita tumefungua duka Masenze.”

Kwa upande wake Tarik Nassoro ambaye ni Mkurugenzi wa NASSCO ambayo Wakala wa Oryx Gas amesema kwa kushirikiana na Oryx wamefungua maduka katika maeneo mengi wilayani Ilala huku akiwaomba Watanzania kuendelea kutumia gesi ya oryx na waache kutumia nishati ambazo zinachafua mazingira .

Wakati huo huo Baba Lishe Dickson Kuga na Mama Lishe Beatrice Shayo wametoa rai kwa mama na baba lishe nchini kutumia nishati safi ya kupikia katika kuandaa chakula kwani nishati safi inaokoa muda lakini pia haina madhara kiafya kama wakitumia kuni na mkaa.








Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir,akizungumza wakati akifunga Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo leo Aprili 30,2026 jijini Dodoma.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir,akizungumza wakati akifunga Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo leo Aprili 30,2026 jijini Dodoma.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir,akizungumza wakati akifunga Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo leo Aprili 30,2026 jijini Dodoma.

Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo,akizungumza wakati wa   Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo uliofanyika leo Aprili 29,2029 jijini Dodoma.

Sehemu ya washiriki wakisikiliza Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir (hayupo pichani) wakati akifunga Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo leo Aprili 30,2026 jijini Dodoma.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir,akiwa katika picha ya pamoja wakati akifunga Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo leo Aprili 30,2026 jijini Dodoma.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir,akiwa katika picha ya pamoja wakati akifunga Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo leo Aprili 30,2026 jijini Dodoma.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir,akiwa katika picha ya pamoja wakati akifunga Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo leo Aprili 30,2026 jijini Dodoma.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir,akiwa katika picha ya pamoja wakati akifunga Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo leo Aprili 30,2026 jijini Dodoma.

......

Serikali imewataka watumishi wa sekta ya elimu nchini kuimarisha mshikamano, uwajibikaji na ubunifu ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa elimu bora inayokidhi mahitaji ya karne ya 21.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir wakati akifunga Mkutano wa Pili wa Baraza la 37 la Wafanyakazi wa Wizara hiyo uliofanyika leo Aprili 30,2026 jijini Dodoma.

Mhe.Ameir  amesisitiza kuwa mafanikio ya sekta ya elimu yanategemea kwa kiasi kikubwa ushirikiano kati ya wafanyakazi, menejimenti pamoja na wadau wote wa elimu, akibainisha kuwa mshikamano huo ni chachu ya kuleta mageuzi chanya na endelevu.

Ametoa pongezi kwa uongozi wa Wizara, ukiongozwa na Waziri Adolf Mkenda, kwa kuendelea kusimamia mageuzi ya elimu ikiwemo maboresho ya sera na mitaala inayolenga kuendana na maendeleo ya sayansi na teknolojia duniani.

Aidha, amempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa uongozi wake unaoendelea kuleta mabadiliko makubwa katika sekta ya elimu, hususan katika kukuza ubora wa elimu, ubunifu na tafiti.

" Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuimarisha elimu, ikiwemo uzinduzi wa Mkakati wa Kisayansi wa Kuimarisha Stadi za Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK) pamoja na mpango wa kuunganisha taasisi za elimu na waajiri."amesema Mhe.Ameir

Ameeleza kuwa mipango hiyo inalenga kuwajengea wanafunzi ujuzi unaoendana na mahitaji ya soko la ajira na hivyo kuongeza ushindani wao kitaifa na kimataifa.

Hata hivyo amewataka wajumbe wa baraza hilo kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za utumishi wa umma, akisisitiza umuhimu wa kuwa na maadili, nidhamu na uwajibikaji kazini.

Amebainisha kuwa baraza la wafanyakazi limeendelea kuwa jukwaa muhimu la majadiliano, ushauri na maamuzi yanayochangia kuboresha utendaji kazi pamoja na ustawi wa watumishi.

Katika mkutano huo, mada mbalimbali zilijadiliwa ikiwemo bajeti ya wizara, usimamizi wa rasilimali watu, maadili ya utumishi wa umma na afya ya akili mahali pa kazi.

Ameir amesema  mada hizo zina mchango mkubwa katika kuboresha mazingira ya kazi na kuongeza tija kwa watumishi, hivyo kuimarisha utoaji wa huduma bora kwa wananchi.

Aidha Ameir ametoa wito kwa watumishi wote kuendelea kudumisha mshikamano, uzalendo na uadilifu, pamoja na kuwa mabalozi wa kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa elimu.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Prof.Carolyne Nombo, amesema kuwa utekelezaji wa kaulimbiu ya mkutano wa wafanyakazi ya “Ushirikishwaji na Mshikamano wa Wafanyakazi ni Chachu ya Kuimarisha Elimu Inayochochea Ubunifu” ni muhimu katika kufanikisha malengo ya sekta ya elimu nchini.

Prof. Nombo amesisitiza kuwa mshikamano na ushirikiano kazini ni msingi wa kuleta mabadiliko ya kweli katika sekta ya elimu.

Ameeleza kuwa kaulimbiu hiyo inalenga kuwajenga watumishi kuwa na utamaduni wa kufanya kazi kwa pamoja, kwa bidii na kwa uwajibikaji, hali ambayo itachochea mageuzi makubwa yanayohitajika katika kuboresha ubora wa elimu nchini.

“Tunaposhirikiana na kufanya kazi kwa bidii kama timu moja, tunaweka msingi imara wa kuleta mabadiliko chanya katika sekta ya elimu, yanayoakisi dira ya maendeleo ya taifa ya mwaka 2050,” amesema Prof. Nombo.

Ameongeza kuwa juhudi hizo zinapaswa kuendana na utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 (toleo la 2023), pamoja na kuzingatia mabadiliko mbalimbali yaliyofanyika katika mitaala iliyoboreshwa.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa watumishi kuzingatia sheria, kanuni, taratibu na miongozo ya serikali katika kutekeleza majukumu yao, akibainisha kuwa nidhamu na uwajibikaji ni nguzo muhimu za kufanikisha malengo ya wizara.





Na Oscar Assenga, Tanga

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Dkt. Balozi Batilda Burian, amesema mkoa huo umeanza mkakati maalum wa kukuza na kutangaza utalii wa fukwe pamoja na fursa za uwekezaji zilizopo, ili kuongeza mchango wake katika uchumi wa Taifa.

Akizungumza , amesema ameita wadau mbalimbali kwa ajili ya kujadili na kuweka mikakati ya pamoja ya kuitangaza Tanga, akibainisha kuwa mkoa huo umejaliwa kuwa katika ukanda wa Bahari ya Hindi wenye maeneo mengi yenye fursa za kiuchumi na utalii.

Ametaja baadhi ya maeneo hayo kuwa ni pamoja na Kipumbwi (Pangani), Ushongo, Kwale (Mkinga) na maeneo ya Raskazone jijini Tanga, ambapo kuna mradi wa kuboresha fukwe unaofadhiliwa na Benki ya Dunia.

Amesema mradi huo utakapokamilika utafungua fursa za michezo ya maji, matembezi ya boti, kuogelea pamoja na shughuli za kijamii kama harusi.


Aidha, amesema mkoa umeanza kushirikiana na Kampuni ya Makazi Solution pamoja na wadau wa Zanzibar ili kujifunza na kubadilishana uzoefu wa namna ya kuendeleza utalii wa fukwe.

Timu ya wataalamu inatarajiwa kwenda Zanzibar kukutana na Wizara ya Utalii na wadau wengine ili kuimarisha ushirikiano huo.

“Tunajifunza kutoka Zanzibar, ambako maeneo kama Nungwi na Paje yalianza kidogo lakini sasa yamekua vituo vikubwa vya utalii. Sasa ni wakati wa Tanga kuchukua nafasi hiyo,” amesema.

Kwa upande wa uwekezaji, Dkt. Burian ameeleza kuwa mradi wa Kipumbwi Satellite City, unaotekelezwa kwa ushirikiano na Halmashauri ya Pangani na Makazi Solution, unalenga kutoa fursa kwa wananchi na wawekezaji kupata viwanja na kuendeleza eneo hilo.


Amesema eneo la Kipumbwi lina umuhimu mkubwa kimkakati, likiwa kilomita 3 kutoka bandari ya Kipumbwi, kilomita 80 kutoka Tanga, kilomita 60 kutoka Zanzibar kwa njia ya bahari, na kilomita 180 kutoka Dar es Salaam. Pia ujenzi wa barabara ya Tanga–Pangani–Saadani–Bagamoyo unatarajiwa kufungua zaidi ukanda huo wa pwani.

Mbali na fukwe, mkoa wa Tanga una vivutio vingi vya utalii ikiwemo Mapango ya Amboni, Hifadhi ya Taifa ya Saadani, Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi, Milima ya Usambara (Lushoto), pamoja na urithi wa kihistoria kama makaburi ya vita ya kwanza ya dunia na Kisiwa cha Toten.

Ameongeza kuwa Tanga pia ni kitovu cha utamaduni wa Kiswahili, likiwa na historia ya muziki wa taarab, vyakula vya asili, pamoja na kuwa chimbuko la lugha ya Kiswahili, ambapo mwanazuoni mashuhuri Sheikh Shaban Robert alizaliwa katika eneo hilo.

Kwa sasa, amesema mkoa unapokea wageni kutoka ndani na nje ya nchi, hususan kutoka Kenya, Ujerumani, Uholanzi na Uswisi, wanaovutiwa na historia, mazingira asilia na utamaduni wa Tanga.

Dkt. Burian amesema jitihada hizo zinaunga mkono azma ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kuitangaza Tanzania kupitia kampeni ya Royal Tour na kuongeza idadi ya watalii.

Kwa upande wa uchumi, amesema mkoa wa Tanga kwa sasa unachangia takribani shilingi trilioni 9.8 katika pato la taifa, na una mpango wa kuongeza mchango huo na kufikia nafasi ya pili kitaifa baada ya Dar es Salaam ifikapo mwaka 2028.

Amehitimisha kwa kusema kuwa Tanga ni eneo sahihi kwa uwekezaji na utalii, akiwakaribisha wawekezaji na watalii kutoka ndani na nje ya nchi kuja kutumia fursa zilizopo.Kwa upande wake Afisa Mahusiano kutoka Kampuni ya Makazi Solution(T) Limited Maximilian Lukosi amesma dhamira yako kubwa ni kuufanya mkoa wa Tanga kuwa daraja la watalii ili wakitokea Zanzibar wapiti hapa na ndio waelekee mikoa mingine ikiwemo Kilimanjaro na Arusha

Wananchi na Wamiliki wa Ardhi Mkoani Kagera wametakiwa kulupia Kodi ya Ardhi kwa wakati ili kuepuka Usumbufu na Migogoro inayoweza kujitokeza.

Wito huu umetolewa na Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Kagera, Ndugu Erick Peter Makundi, kwa wananchi wa Mkoa huo kuhakikisha wanalipa kodi ya pango la ardhi kwa wakati ili kuepuka malimbikizo pamoja na usumbufu unaoweza kujitokeza baadaye, na kusisitiza kuwa ulipaji wa kodi hiyo si hiari, bali ni wajibu wa kila mmiliki wa ardhi, na unachangia moja kwa moja katika kuboresha huduma za kijamii zinazotolewa na Serikali.

Akizungumza na waandishi wa habari Ofisini kwake Aprili 29 mwaka huu, Makundi ameeleza kuwa Serikali imeweka sheria madhubuti kwa wadaiwa sugu wa kodi ya ardhi. 

Hata hivyo amebainisha kuwa hatua zinazoweza kuchukuliwa ni pamoja na kufutiwa hati za umiliki wa ardhi au hata kuchukuliwa hatua za kisheria mahakamani. Hivyo, kuwataka wananchi kutekeleza wajibu wao kwa hiari ili kuepuka madhara hayo.

Kwa upande mwingine, Makundi alifafanua kuwa iwapo wananchi wote wanaodaiwa watalipa kodi hiyo kwa wakati, zaidi ya shilingi bilion 20 zinaweza kukusanywa, jambo litakaloongeza mapato ya serikali na kusaidia maendeleo ya kijamii na kiuchumi. 

Pia alitaja baadhi ya changamoto wanazoweza kukutana nazo wadaiwa, ikiwa ni pamoja na kushindwa kutumia hati zao za ardhi kupata mikopo au kuzitumia kama dhamana hadi watakapomaliza kulipa madeni yao.

Baadhi ya wananchi waliopata nafasi ya kutoa maoni yao wamesema kuwa wamepokea wito huo kwa mtazamo chanya, huku wakieleza kuwa wako tayari kutimiza wajibu wao kwa kulipa kodi kwa wakati huku wakiiomba  serikali kuendelea kutoa elimu zaidi kuhusu umuhimu wa kodi ya ardhi pamoja na kuboresha mifumo ya ulipaji ili iwe rafiki na rahisi kwa kila mwananchi kuitumia bila changamoto.






Na Immaculate Makilika - MAELEZO

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Paul Makonda amewataka wadau wa sekta ya habari kubadili ajenda ya kutangaza watu badala yake watangaze fursa za uchumi zilizopo nchini.

Ametoa rai hiyo leo Aprili 30, 2026 katika Siku ya Tatu ya Maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani iliyofanyika jijini Arusha.

“ Tuache ajenda ya kutangaza watu, tuitangaze nchi yetu. Tubadilishe mkakati kutoka ajenda ya kusifia watu, tuambieni fursa za uchumi zilizopo,” amesema Waziri Makonda

Ameongeza kuwa waandishi wa habari waache kasumba ya kuwaandika vizuri wala rushwa na watu wasio na sifa njema katika jamii, badala yake wafanye kazi zao kwa maslahi ya Taifa.

Ametolea mfano kuwa hakuna idadi ya kutosha ya waandishi wanaoandika kuhusu sekta ya utalii au kilimo kama wanaoandika kuhusu masula ya siasa.

Amezungumzia kuhusu Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 na kuwaasa waandishi wa habari kushiriki kikamilifu ili kufikia malengo yaliyowekwa huku akisisitiza kuhusu umuhimu wa mchango wa Vvyombo vya Habari kwa maendeleo ya nchi.

Aidha, Waziri Makonda amewataka waandishi wa habari kujiridhisha na vyanzo vya taarifa za kabla ya kuzisambaza kwa umma ili kuepuka upotoshaji na migogoro.

Kuhusu mapendekezo yaliyotelewa na wadau wa sekta ya habari ya kuboresha utendaji wa sekta hiyo nchini, Mhe. Makonda amesema Serikali imeyapokea mapendekezo yote 15 na itayafanyia kazi kwa kushirikiana na wadau.

Naye, Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Bw. Gerson Msigwa amesema kuwa lengo la Maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani ni kutathimi na kulinda hali ya uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani.

Ameongeza kuwa kupitia Maadhimisho hayo Serikali itapata fursa ya kukutana na washirika wake wa maendeleo na asasi za kiraia kujadili masuala ya mabadiliko ya utendaji kazi katika sekta ya habari pamoja na kuwaendeleza watayarishaji wa maudhui.

Naye, Mkurugenzi wa Taasisi ya Tech and Media Convergency (TMC) na Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Maadhimisho hayo kwa mwaka 2026, Bi. Asha Abinallah amesema kuwa kupitia Maadhimisho hayo wadau wameandaa mapendekezo kadhaa ikiwemo kuitaka Serikali kuharakisha uanzishwaji wa Mfuko wa Habari na kuandaa sera rafiki za kuvutia uwekezaji katika sekta ya habari.

Vilevile, wameitaka Serikali kupitia Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) kuendelea kutimiza majukumu yake ikiwemo kuwajengea uwezo wanahabari katika matumizi ya akili unde.










MAHAKAMA Kuu Masijala Ndogo Dar es salaam, imetupilia mbali maombi ya Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Tundu Lissu ya kuomba kuunganishwa katika kesi ya mgawanyo wa mali iliyofunguliwa na Makamu Mwenyekiti wa chama hicho Zanzibar, Said Issa Mohamed, pamoja na wenzake.

Wengine waliofungua kesi hiyo hiyo ni wajumbe wa bodi ya wadhamini wa Zanzibar Ahmed Rashid Khamis na Maulidah Anna Komu (marehemu).

Wajibu maombi katika kesi hiyo namba 8323 ya mwaka 2025  ambao ni Bodi ya Wadhamini ya Chadema upande wa bara na Katibu Mkuu wa chama hicho, John Mnyika.

Uamuzi huo mdogo umetolewa na Jaji Hamidu mwanga ambaye awali alikuwa akikisikikiza shauri hilo na umesomwa leo Aprili 30, 2026  na Naibu Msajili ya Mahakama hiyo, Hussein Mushi.

Awali, kesi hiyo ilikuwa ikisikilizwa mbele ya Jaji Mwanga kama ilivyoelezwa, huku Lissu aliomba kuunganishwa katika kesi hiyo akidai kuwa kwakuwa kesi hiyo inahusu chama na yeye ndiye mwenyekiti wa chama basi anapaswa kuwa sehemu ya kesi hiyo.

Maombi hayo yalisikilizwa na uamuzi ulipaswa kutolewa Machi 25, mwaka huu lakini kutokana na faili kuitwa Mahakama ya Rufaa Dodoma kesi hiyo ilipelekwa mbele hadi leo.

Katika uamuzi huo Mahakama imekataa kumuunganisha Lissu katika kesi hiyo kama mwenyekiti wa Chama lakini kwakuwa ameyapeleka kwa matakwa yake na si kwa nafasi yake hivyo hana maslahi ya moja kwa moja kwani cheo hicho kinaweza kukaliwa na mtu yeyote

Mahakama imeeleza kuwa Lissu anaweza kutokea kwenye kesi hiyo kama shahidi wakati wa usikilizwaji wa kesi ya msingi na si kama moja ya wajibu maombi

Akizungumza nje ya Mahakama Wakili wa chadema , Dkt. Rugemeleza Nshala amedai kesi hiyo kwa sasa imehamishiwa kwa Jaji David Ngunyale na inatarajiwa kutajwa Mei 13,2026.

"Kurudi kwa kesi hii kunaenda sambamba na kufuata maagizo ya mahakama ya Rufaa ya kumtaka Jaji huyo kuangalia kama maombi hayo yalipelekwa ndani ya muda au laa.

“Madai yanatakiwa yaletwe ndani ya miaka sita tangu kuanza kwa migogoro katika uamuzi wa leo wa Jaji Mwanga wakili wa upande wa walalamikaji alisema kwa msisitizo kwamba mgogoro ulianza mwaka 2016, hivyo jaji Ngunyale atatusaidia kuangalia ni muda gani kati ya 2016 hadi 2025,” ameeleza Dkt. Nshala.

Akizungumzia kesi ya uhaini dhidi ya Lissu,  Dkt Nshala bado hawajajua itapangwa lini kwa sababu kesi hiyo ipo katika Mahakama ya rufaa ambayo ndo inatarajiwa ipange mara nyingi hupangwa kwa muundo wa vikao, hivyo msajili wa Mahakama ya rufaa ndiyo atajua ipangwe lini,” amedai Dkt Nshala.





Na. Mwandishi Wetu, Morogoro

Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi imetoa wito kwa watendaji wa uchaguzi kuhakikisha wanatumia muda wao kusoma Katiba, sheria za uchaguzi, kanuni na maelekezo ya Tume ili waweze kusimamia uchaguzi kwa weledi.

Wito huo umetolewa na Makamu Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa (Mst) Mbarouk Salim Mbarouk Mkoani Morogoro leo tarehe 30 Aprili, 2026 wakati akifunga mafunzo ya watendaji wa uchaguzi yaliyofanyika kwa siku tatu kuanzia tarehe 28 Aprili, 2026.

Mafunzo hayo ni sehemu ya mchakato wa maandalizi ya uchaguzi mdogo wa ubunge kwenye Jimbo la Ismani Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, Mkoani Iringa na Kata 12 za Tanzania Bara unaotarajiwa kufanyika tarehe 01 Juni, 2026.

“Natumia nafasi hii kuendelea kuwasisitiza kuhusu umuhimu wa kutenga sehemu ya muda wenu kusoma Katiba, sheria na maelekezo mbalimbali yanayotolewa na Tume ili yawaongoze katika kusimamia uchaguzi utakaokuwa huru na wa haki,” amesema Jaji Mbarouk.

Amewataka watendaji hao wa uchaguzi kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na weledi ili kufanikisha uchaguzi huo mdogo ambao unafanyika kujaza nafasi wazi ya mbunge na madiwani.

“Jukumu lililopo mbele yetu ni kubwa na muhimu, linahitaji umakini na kujituma. Ni matazamio ya Tume kwamba, baada ya kupatiwa mafunzo haya, mtatekeleza majukumu yenu kwa ufanisi na weledi mkizingatia ratiba ya utekelezaji ili kufanikisha uchaguzi mdogo wa ubunge katika Jimbo la Ismani na Kata 12 za Tanzania Bara unaotarajiwa kufanyika tarehe 01 Juni, 2026,” amesema Jaji Mbarouk.

Amesisitiza kuwa ili ufanisi uwepo ni muhimu watendaji hao wazingatie sifa na uwezo wakati wa kuteua na kuajiri watendaji wa vituo vya kupigia kura kwa kuwa hao ndio watakaosimamia zoezi la kupiga kura na kuhesabu kura vituoni.

“Kuhusu ajira za watendaji wa vituo, tunayo imani kuwa mtateua na kuajiri watendaji wenye sifa na uwezo wa kufanya kazi hii muhimu kwa kuwa hao ndio watakaosimamia zoezi la kupiga kura na kuhesabu kura vituoni. Kazi ambayo inahitaji umahiri, umakini na weledi katika kuitekeleza.,” amesema Jaji Mbarouk.

Amewataka watendaji hao kuhakikisha kuwa mafunzo ya watendaji wa vituo yanafanyika kwa ufanisi na weledi katika tarehe zilizopangwa kwenye ratiba ya utekelezaji wa shughuli za uchaguzi.

Ameongeza kuwa mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo ili waweze kufahamu majukumu yao na kuyatekeleza ipasavyo wakati wa uchaguzi.

Mafunzo hayo yamewahusisha Waratibu wa Uchaguzi wa Mikoa, Wasimamizi wa Uchaguzi, Wasimamizi Wasaidizi wa Uchaguzi Ngazi ya Jimbo, Wasimamizi wa Uchaguzi Ngazi ya Kata, Maafisa Uchaguzi, Maafisa Ununuzi na Wahasibu.

Kata 12 za Tanzania Bara zitakazofanya uchaguzi wa Udiwani ni Mzimuni iliyopo Manispaa ya Kinondoni; Zongomera, Manispaa ya Kahama; Itilo, Halmashauri ya Mji wa Nzega; Ketare, Halmashauri ya Mji wa Tarime na Nyumbigwa, Halmashauri ya Mji wa Kasulu.

Nyingine ni kata ya Kala iliyoko Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi; Ziba, Halmashauri ya Wilaya Igunga; Kamsisi, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele; Nyamugali, Halmashauri ya wilaya ya Buhigwe; Namasakata Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru; Bwongera, Halmashauri ya Wilaya ya Chato na Kibiti Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti.
Makamu Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa (Mst) Mbarouk Salim Mbarouk akizungumza wakjati akifunga mafunzo ya watendaji wa uchaguzi yaliyofanyika Mkoani Morogoro. Mafunzo hayo yamefungwa leo tarehe 30 Aprili, 2026 na yaliyofanyika kwa siku tatu kuanzia tarehe 28 Aprili, 2026. (Picha na INEC). 
Sehemu ya watendaji wa uchaguzi katika jimbo la Isimani Mkoani Iringa na Kata 12 za Tanzania bara wakisikiliza hotuba ya kufunga mafunzo ya siku tatu yaliyofanyika mkoani Morogoro kuanzia tarehe 28 hadi 30 Aprili, 2026. (Picha na INEC).





Na Janeth Raphael- MichuziTv -Dodoma 

Serikali imesema imepokea rasmi ushauri wa wabunge kuhusu kuanzishwa kwa mfumo wa bima ya afya kwa wakulima, hususan wale wanaojihusisha na zao la korosho, huku ikiweka wazi kuwa tayari imeanza mchakato wa kufanya tathmini ya kina ili kubaini namna bora ya kutekeleza mpango huo.

Akizungumza bungeni jijini Dodoma Aprili 29, 2026 wakati akijibu hoja zilizotolewa na wabunge katika mjadala wa bajeti ya Wizara ya Kilimo kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo, amesisitiza kuwa Serikali inatambua umuhimu wa pendekezo hilo na inalipa uzito unaostahili kutokana na mchango mkubwa wa wakulima katika uchumi wa taifa.

Ameeleza kuwa hatua ya awali ni kufanya uchambuzi wa kina utakaosaidia kubaini muundo sahihi wa bima hiyo, ikiwemo gharama, walengwa, na namna ya kuisimamia ili iweze kuwa endelevu na yenye manufaa kwa wakulima.

“Hoja ya bima ya afya kwa wakulima wa korosho tumeipokea. Tunakwenda kufanya tathmini ya kina ili kujua namna bora ya kuitekeleza. Baada ya hapo, tutakaa na wadau mbalimbali kuona jinsi ya kuanzisha mpango huo kwa ufanisi,” alisema Chongolo.

Aidha, Waziri huyo amebainisha kuwa mpango huo hautalenga wakulima wa korosho pekee, bali Serikali inalenga kuupanua ili kuwahusisha wakulima wa mazao mengine ya kimkakati kama pamba, tumbaku na mazao mengine yanayolimwa kwa wingi nchini.

Chongolo amesema kuwa lengo kuu la mpango huo ni kuboresha ustawi wa wakulima kwa kuwapatia kinga ya kiafya, jambo litakalowasaidia kufanya kazi zao kwa ufanisi zaidi na hatimaye kuongeza tija katika sekta ya kilimo.

Hatua hiyo inatajwa kuwa sehemu ya jitihada za Serikali za kuimarisha sekta ya kilimo, ambayo ni mhimili muhimu wa uchumi wa nchi, pamoja na kuhakikisha kuwa wakulima wanapata huduma bora za kijamii zinazowawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji.

Wadau wa sekta ya kilimo wamekuwa wakisisitiza umuhimu wa kuwepo kwa mifumo ya hifadhi ya jamii kwa wakulima, wakieleza kuwa changamoto za kiafya mara nyingi huathiri uzalishaji na kipato chao. Kupitia mpango huu unaopendekezwa, inatarajiwa kuwa wakulima watanufaika kwa kupata huduma za afya kwa gharama nafuu au kwa mfumo unaowawezesha kumudu kulipia huduma hizo kwa urahisi zaidi.





Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma

Serikali kupitia Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari imeweka wazi mkakati wake wa kuendeleza sekta ya TEHAMA kwa kuwasilisha bungeni makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha 2026/2027. Bajeti hiyo inalenga kuimarisha miundombinu ya mawasiliano pamoja na kukuza uchumi wa kidijitali nchini.

Akiwasilisha taarifa hiyo, Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Angellah Kairuki, amesema wizara inatarajia kukusanya jumla ya Shilingi 160,369,240,000. Mapato hayo yanatarajiwa kutokana na uuzaji wa huduma za Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano, ambao umeendelea kupanuka na kuongeza matumizi ndani na nje ya mipaka ya nchi.

Amesema kuwa ongezeko la makusanyo linachochewa na kuimarika kwa matumizi ya huduma za mawasiliano, sambamba na juhudi za serikali kueneza miundombinu ya intaneti hadi maeneo zaidi ya vijijini na mijini. Hatua hiyo inalenga kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanapata huduma bora na za uhakika.

Kwa upande wa matumizi, wizara imeomba kuidhinishiwa jumla ya Shilingi 222,589,451,000 kwa ajili ya kutekeleza majukumu yake katika mwaka ujao wa fedha. Kiasi hicho kinajumuisha matumizi ya kawaida na fedha za miradi ya maendeleo.

Kati ya fedha hizo, Shilingi 13,146,172,000 sawa na asilimia 5.9 ya bajeti yote zimetengwa kwa matumizi ya kawaida. Ndani ya fungu hilo, Shilingi 6,371,830,000 ni kwa ajili ya mishahara ya watumishi, huku Shilingi 6,774,342,000 zikielekezwa kwenye gharama nyingine za uendeshaji wa wizara.

Sehemu kubwa ya bajeti hiyo, ambayo ni Shilingi 209,443,279,000 sawa na asilimia 94.1, imeelekezwa katika miradi ya maendeleo. Mgawanyo wa fedha hizo unaonesha kuwa Shilingi 98,480,905,000 ni fedha za ndani, wakati Shilingi 110,962,374,000 zitatoka kwa washirika wa maendeleo kutoka nje ya nchi.

Waziri Kairuki amesisisitiza kuwa uwekezaji huu mkubwa utaongeza upatikanaji wa huduma za mawasiliano, kuboresha kasi na ubora wa intaneti, pamoja na kufungua fursa mpya za kiuchumi kupitia teknolojia. Aidha, utawezesha sekta mbalimbali kama elimu, afya na biashara kunufaika zaidi na mapinduzi ya kidijitali.

Kwa ujumla, bajeti hiyo inalenga kuharakisha mageuzi ya kidijitali nchini, kuongeza ufanisi wa huduma za umma, na kuiweka Tanzania katika nafasi nzuri ya ushindani wa kiteknolojia ndani ya ukanda na kimataifa.


 

KATIBU Mkuu wa Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira Tanzania(TRAMEPRO) Boniventura Mwalongo amekutana na kufanya mazungumzo na Chifu Msangia Ongati Ngoje wa Rorya ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa Machifu na Mzee wa Mila na Desturi Mkoa wa Mara.

Kikao hicho kilijikita katika kujadili mustakabali wa taifa letu, hususan katika maeneo ya utatuzi wa migogoro ya ardhi, maadili ya jamii, uadilifu katika utumishi wa umma, pamoja na dira ya maendeleo ya muda mrefu ya Tanzania.

Taarifa ya Makamu Mwenyekiti wa Machifu na Mzee wa Mila na Desturi Mkoa wa Mara Chifu Msangia Ongati Ngoje amesema katika kikao hicho, wamekubaliana kuimarisha nafasi ya mila na desturi katika utatuzi wa migogoro ya ardhi, kurejesha na kuendeleza maadili na uadilifu katika jamii na taasisi za umma.

Pia kujenga taifa lenye umoja, uwajibikaji na matumizi bora ya rasilimali. Aidha, walisisitiza umuhimu wa kuendeleza sekta ya tiba asili kama nyenzo ya afya na uchumi, na kulinda pamoja na kuendeleza utamaduni wa Waluo kama urithi muhimu wa taifa.

Amesena kama alivyosema mwanafalsafa mashuhuri William Shakespeare, “Ujinga ni laana; maarifa ni mabawa yanayotuinua juu.” ambapo nukuu hiyo inatukumbusha umuhimu wa sayansi, maarifa na elimu katika kuleta maendeleo endelevu ya jamii. 

Pia amesema, “Mguso mmoja wa asili huwafanya watu wote kuwa ndugu,” akisisitiza nafasi ya mazingira katika kuunganisha binadamu wote. 

Aidha, katika kuelezea maisha ya jamii na utamaduni wake, alisema, “Maisha yetu yamefumwa kwa nyuzi mchanganyiko—mema na mabaya pamoja,” jambo linalotukumbusha wajibu wa kuhifadhi mema ya utamaduni wetu na kurekebisha kasoro zilizopo.

Kwa upande wa uongozi wa kitaifa, amesema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewahi kusisitiza kuwa, “Mila na desturi zetu ni utambulisho wetu kama taifa, ni wajibu wetu kuzilinda, kuziheshimu na kuzitumia kama chachu ya maendeleo endelevu.” 

Kauli hiyo inaonesha dhamira ya serikali katika kuendeleza urithi wa kitamaduni sambamba na maendeleo ya kisasa.

Kwa upande wa maendeleo ya eneo, Shirati ni Halmashauri ya Mji Mdogo iliyopo katika Wilaya ya Rorya, Mkoa wa Mara, Kaskazini mwa Tanzania, karibu na mpaka wa Kenya na kandokando ya Ziwa Victoria. 

“Mji huu unakadiriwa kuwa na wakazi kati ya 50,000 hadi 100,000, huku Wilaya ya Rorya ikiwa na takribani wakazi 354,490 kwa mujibu wa Sensa ya mwaka 2022. Idadi kubwa ya wakazi ni vijana wanaoishi vijijini.

“Shughuli kuu za kiuchumi katika eneo hili ni pamoja na kilimo kinachotegemewa na zaidi ya asilimia 80 ya wananchi, kikijumuisha mazao ya mahindi, mihogo, mtama, alizeti na pamba. 

“Uvuvi pia ni shughuli muhimu inayofanyika katika Ziwa Victoria ukihusisha samaki kama sangara, sato na dagaa. Aidha, wananchi hujihusisha na ufugaji wa ng’ombe, mbuzi na kondoo pamoja na biashara ndogo ndogo, ikiwemo biashara za mipakani kati ya Tanzania na Kenya.”

Amesema Kijiografia, eneo la Shirati liko katika Mkoa wa Mara, kaskazini mwa Tanzania, karibu na mpaka wa Kenya na kuzungukwa na Ziwa Victoria, likiwa na hali ya hewa ya kitropiki yenye mvua za msimu. Hali hii huchangia kwa kiasi kikubwa shughuli za kiuchumi na maisha ya wananchi wa eneo hilo.

Amesema utamaduni wa Waluo unaendelea kuwa nguzo muhimu ya mshikamano wa jamii, ukijengwa juu ya heshima kwa wazee na viongozi wa mila, matumizi ya baraza la wazee katika utatuzi wa migogoro, mshikamano wa kifamilia na kijamii, pamoja na kuzingatia maadili ya uadilifu, uwajibikaji na upendo. 

Pamoja na hayo amesema ni wazi  ushirikiano kati ya viongozi wa mila na desturi, serikali, wataalamu na wananchi ni muhimu katika kujenga jamii yenye maadili imara, uchumi thabiti na maendeleo endelevu. 

“Tunatoa mwito kwa wadau wote kushiriki kikamilifu katika kulinda mazingira, kuendeleza tiba asili, kuhifadhi utamaduni wa Waluo na kutumia vyema fursa zilizopo kwa maendeleo ya Mkoa wa Mara na taifa kwa ujumla,”amesema Chifu Msangia Ongati Ngoje wa Rorya. 


Top News