Na Munir Shemweta, WANMM


Watumishi wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Makao Makuu wamepatiwa mafunzo maalum ya lishe pamoja na mwongozo wa kudhibiti VVU/ UKIMWI na magonjwa yasiyoambukizwa, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuwaimarisha kiafya na kuongeza ufanisi wao kazini.

Mafunzo hayo ya siku moja yamefanyika tarehe 27 Machi, 2026 katika ofisi za wizara zilizopo Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma, yakilenga kuwajengea watumishi uelewa mpana kuhusu namna bora ya kujikinga na magonjwa pamoja na kuzingatia lishe bora katika maisha ya kila siku.

Akifungua mafunzo hayo, Kaimu Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa wizara hiyo, Bw. Deodatus Mwiliko, alisema kuwa afya ya mtumishi ni nyenzo muhimu katika kuongeza tija na ufanisi kazini, hivyo ni muhimu kwa watumishi kupewa elimu sahihi ya afya mara kwa mara.

Alieleza kuwa, Wizara ya Ardhu, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imejipanga kuhakikisha watumishi wake wanapata mafunzo mbalimbali yanayogusa ustawi wao, ikiwemo masuala ya afya, ili kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi.

Katika mafunzo hayo, mada kuhusu mwongozo wa kudhibiti VVU/UKIMWI na magonjwa yasiyoambukizwa iliwasilishwa na Bi. Juliana Ntukey kutoka Ofisi ya Rais – Utumishi, ambaye alisisitiza umuhimu wa kuzingatia miongozo iliyopo ili kulinda afya za watumishi na jamii kwa ujumla.

Aidha, mada ya lishe bora iliwasilishwa na Bi. Semeni Eva Juma, Afisa Lishe kutoka Jiji la Dodoma, ambapo alitoa elimu juu ya umuhimu wa kula mlo kamili na wenye virutubisho vinavyohitajika kwa afya bora ya mwili.

Kwa ujumla, mafunzo hayo yamepokelewa kwa hamasa kubwa na watumishi, huku yakitarajiwa kuwa chachu ya mabadiliko chanya katika kuimarisha afya na ustawi wao mahali pa kazi.
Bi. Juliana Ntukey kutoka Ofisi ya Rais – Utumishi akitoa mafunzo kuhusu muongozo wa kudhibiti VVU/Ukimwi na magonjwa sugu zyasiyoambukizwa kwa watumishi wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi jijini Dodoma tarehe 27 Machi 2026.







Sehemu ya watumishi wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi wakiwa katika mafunzo maalum ya lishe pamoja na mwongozo wa kudhibiti VVU/UKIMWI na magonjwa yasiyoambukizwa yaliyofanyika jijini Dodoma tarehe 27 Machi, 2026.
Bi. Juliana Ntukey kutoka Ofisi ya Rais – Utumishi akitoa mafunzo kuhusu muongozo wa kudhibiti VVU/Ukimwi na magonjwa sugu zyasiyoambukizwa kwa watumishi wa Wizara ya Ardhi Jijini Dodoma tarehe 27 Machi 2026.

Bi. Semeni Eva Juma, Afisa Lishe kutoka Jiji la Dodoma, akitoa elimu juu ya umuhimu wa kula mlo kamili na wenye virutubisho vinavyohitajika kwa afya bora ya mwili kwa watumishi wa wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi jijini Dodoma tarehe 27 Machi, 2026.






Baadhi ya watumishi wa Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi wakiwa katika mafunzo maalum ya lishe pamoja na mwongozo wa kudhibiti VVU/UKIMWI mahala pa kazi tarehe 27 Machi 2026 (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)








DODOMA: Katibu Mkuu wa Shirika la TRAMEPRO, Boniventura Mwalongo, ametoa pole kwa familia ya marehemu William V. Lukuvi jijini Dodoma, akisisitiza kuwa kifo si mwisho wa mwanadamu bali ni mwanzo wa kumbukumbu ya milele kupitia matendo mema.
Akizungumza baada ya kusaini kitabu cha maombolezo, Mwalongo alieleza kuwa urithi wa uongozi wa busara, utulivu, na utetezi wa haki aliouacha marehemu Lukuvi ni alama isiyofutika moyoni mwa jamii. Alibainisha kuwa mchango wa marehemu katika kulinda mazingira na kutumikia wananchi ndio utakaomfanya aishi daima katika historia ya taifa.
Ujumbe huo umetoa funzo kwa viongozi na jamii kuwa thamani ya maisha ya mtu haipimwi kwa muda aliokaa duniani, bali kwa athari chanya aliyoacha kwa wengine. Mwalongo alihitimisha kwa kusema kuwa ingawa mwili umetutoka, misingi na kazi za marehemu Lukuvi zitabaki kuwa mwongozo kwa kizazi cha sasa na kijacho.
.Imetolewa na:
Boniventura Mwalongo
Katibu Mkuu – TRAMEPRO




 

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo ikiongozwa na Mwenyekiti, Mhe. Deodatus Mwanyika (Mb), imeridhia Randama ya mpango wa bajeti ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Viwanda na Biashara kwa mwaka wa fedha 2026/2027 Machi 26, 2027 Bungeni jijini Dodoma

Katika michango yao, Wajumbe wa Kamati hiyo walionyesha kuridhishwa na vipaumbele vya Mpango wa Bajeti hiyo ya mwaka 2026/2027, huku wakimpongeza Waziri Kapinga kwa uwasilishaji wenye maono mapana yanayolenga kukuza sekta ya viwanda na biashara nchini. Pamoja na pongezi hizo, Kamati ilitoa miongozo na ushauri wa kimkakati uliolenga kuboresha mazingira ya biashara, na viwanda nchini.

Naye, Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga (Mb), alibainisha kwa kina kuwa vipaumbele vya kimkakati vitakavyopewa uzito katika Mpango wa bajeti wa 2026/2027, pamoja na mchanganuo wa fedha zinazohitajika kutekeleza majukumu hayo.

Uidhinishaji wa makadirio hayo unafungua milango kwa Wizara ya Viwanda na Biashara kuanza maandalizi ya mwisho ya Hotuba ya Bajeti itakayowasilishwa rasmi na katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Mkutano wa bajeti.

       

 

TUME  ya Ushindani (FCC) kupitia Kanda ya Ziwa imeendelea kusogeza huduma karibu na wananchi kwa kutoa elimu ya ulinzi wa mlaji kupitia Kliniki ya Mlaji inayofanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi Mkendo, Manispaa ya Musoma.

Katika kuimarisha uelewa wa wadau mbalimbali, FCC haikuishia kwa wananchi pekee bali pia ilifanya ziara maalum kwa baadhi ya taasisi zinazotoa huduma ndogo za fedha katika manispaa hiyo, kwa lengo la kuzielimisha juu ya wajibu wao wa kuzingatia sheria na kanuni katika utoaji wa huduma.

Akiongoza zoezi hilo, Mkuu wa Kanda ya Ziwa,Bw. Frank Mdimi, akishirikiana na Afisa Biashara wa Manispaa ya Musoma, Joshua Mlole pamoja na maafisa wengine, walitembelea taasisi za Enokwe, Pongeza na Ohura na kufanya mazungumzo ya moja kwa moja na watoa huduma hao.

Katika ziara hiyo, maafisa wa FCC wamesisitiza umuhimu wa kuandaa mikataba ya huduma kwa uwazi na haki, wakielekeza taasisi hizo kuzingatia matakwa ya  Sheria ya Ushindani inasimamia na kudhibiti Mikataba ya Mlaji inayoandaliwa na watoa huduma

Watoa huduma kutoka taasisi hizo walionesha utayari mkubwa wa kupokea maelekezo hayo, wakieleza kufurahishwa kwao na hatua ya FCC kuwafuata na kuwapatia elimu kwa vitendo. Wamesisitiza kuwa elimu hiyo itawasaidia kuboresha huduma zao na kujenga uaminifu kwa wateja wao.

Aidha, taasisi hizo zimeahidi kushirikiana kwa karibu na FCC kwa kuhakikisha zinazingatia sheria, kanuni na miongozo ya Serikali, pamoja na kudumisha mawasiliano ya mara kwa mara ili kuboresha zaidi sekta ya huduma ndogo za fedha.

Zoezi la utoaji elimu kupitia Kliniki ya Mlaji linaendelea Machi 27, ambapo wananchi wataendelea kupatiwa elimu kuhusu haki zao, wajibu wao na namna bora ya kujilinda wanapotumia huduma mbalimbali sokoni.

NA FARIDA MANGUBE MOROGORO

Katika juhudi za kujenga kizazi chenye uelewa wa masuala ya kodi, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mkoa wa Morogoro ipo kwenye mpango wa kuanzisha vilabu vya kodi (Tax Club) katika shule za sekondari wilayani Kilosa, ikiwa ni hatua muhimu ya kukuza uzalendo na uwajibikaji wa kifedha miongoni mwa wanafunzi.

Meneja wa TRA wilaya ya Kilosa, Laston Makarlu, amesema Tax Club itasaidia kuwajengea wanafunzi uelewa sahihi kuhusu umuhimu wa kodi katika maendeleo ya taifa, ili waweze kuwa walipa kodi waadilifu pindi watakapoingia katika shughuli za kiuchumi. Alibainisha kuwa elimu hiyo itasaidia kuondoa dhana potofu zilizojengeka kwa baadhi ya wananchi kuhusu kodi.

Kwa upande wake, Bi. Emmaculatha Chagu Afisa Mwandamizi wa Elimu na Mawasiliano TRA Morogoro alieleza kuwa utoaji wa elimu ya kodi kuanzia ngazi ya chini ni mkakati sahihi utakaosaidia kujenga uelewa wa kudumu kwa wanafunzi. “Elimu ya mapato lazima ianzie chini ili kuwajenga vijana kuwa raia wanaotambua wajibu wao kwa taifa. Kuanzishwa kwa Tax Club kutawapa wanafunzi nafasi ya kujifunza kwa vitendo na kujenga mtazamo chanya kuhusu ulipaji kodi,” alisema.

Aliongeza kuwa vitakapoanzisha vilabu hivyo vitasaidia pia kukuza uongozi, uwajibikaji na nidhamu miongoni mwa wanafunzi, huku vikitoa jukwaa la majadiliano na ubunifu kuhusu masuala ya uchumi na maendeleo ya nchi.

Pia Tax Club itasaidia kutoa elimu ya msingi kuhusu mfumo wa kodi, wajibu wa mlipa kodi, pamoja na mchango wa kodi katika kugharamia huduma za jamii kama elimu, afya na miundombinu.

Programu hiyo inatarajiwa kutekelezwa katika wilaya zote za Mkoa wa Morogoro, ambapo kwa sasa imeanza kwa kutoa elimu katika Wilaya za Gairo na Kilosa, huku maandalizi yakiendelea kuhakikisha Wilaya zote za mkoa huo yanafikiwa.

Zoezi hilo lilifanyika kwa ushirikiano wa maafisa kutoka TRA mkoa wa Morogoro, ambapo walitembelea shule mbalimbali zikiwemo Kimamba Sekondari na Mazinyungu Sekondari kuzungumza na walimu.






Dar es Salaam 

Serikali kupitia Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) imeanza kutekeleza ujenzi wa barabara Kilomita 42.78 kwa kiwango cha lami kupitia mradi wa Uendelezaji Jiji la Dar es Salaam Awamu ya Pili (DMDP II) katika kata za Mjimwema, Kibada, Kigamboni, Vijibweni na Somangila zilizopo Halmashauri ya Manispaa ya Kigamboni.

Hayo yameelezwa na Kaimu Meneja wa TARURA wilaya ya Kigamboni, Mhandisi Edgar Tumsifu ambapo amesema kuwa mradi huo unaogharimu shilingi Bilioni 110 utekelezaji wake umefikia asilimia 30 huku tayari umeshaanza kuleta matokeo kwani barabara zilizokuwa na changamoto zimeshaanza kufanyiwa kazi na zikikamilika wananchi watanufaika na miundombinu hiyo.

"Tunaishukuru serikali ya Awamu ya Sita chini ya Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutuletea mradi huu, TARURA Kigamboni tuna mtandao wa barabara Km 1035 kati ya hizo barabara za lami ni Km 10 lakini kupitia DMDP II imetuletea Km 42.78 kwahiyo tutakuwa na zaidi ya Km 50 za barabara za lami mpaka kufikia mwezi Agosti mwaka huu", amesema.

Ameeleza kuwa barabara hizo zikikamilika zitasaidia kupunguza uharibifu wa vyombo vya usafiri, pia kuna baadhi ya barabara ambazo ni 'bypass' zikikamilika zitasaidia wakazi wa Kigamboni wanaoelekea maeneo ya Kivukoni au darajani kufika kwa urahisi na haraka. 

"Leo tumetembelea barabara zenye urefu wa Km 10.48 zilizopo kata ya Kibada ambapo utekelezaji wake umefikia asilimia 68, mkandarasi anaendelea na ujenzi wa mitaro na njia za waenda kwa miguu, barabara hizi zikikamilika zitasaidia kupunguza foleni katika maeneo haya", amesema.

Amesema kazi zitakazofanyika katika mradi wa DMDP II ni ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami, njia za waenda kwa miguu, vituo vya daladala, taa za barabarani na mifereji ya maji ya mvua zaidi ya Km 80.

Aidha, amewaomba wananchi wawe watulivu katika kipindi cha mpito cha ujenzi mara baada ya shughuli za ujenzi kukamilika mitaa yote itapendeza na kuwa safi na salama na pia wawe walinzi wa miundombinu hiyo wasitupe taka kwenye mitaro wala wasipitishe magari yenye uzito mkubwa.

Naye, Mwenyekiti wa mtaa wa Kichangani kata ya Kibada, Bw. Nassoro Chande amesema ubovu wa barabara uliokuwepo awali ulikwamisha shughuli zao za kiuchumi na kijamii lakini kwa sasa hali ya kiuchumi itaimarika kufuatia kuendelea kwa ujenzi wa barabara hizo ambazo kwa sasa watu wengi wanajenga maeneo hayo na kufanya thamani ya ardhi kupanda.

Bw. Frank Mwakipageme ambaye ni mfanyabiashara eneo la Shangwe kata ya Kibada amesema kuwa adha kubwa waliyokuwa wanaipata ni maji kujaa hasa kipindi cha mvua kwasababu eneo hilo kuna bonde lakini sasa wamepata nafuu baada ya kutengenezewa mitaro na wanafanya biashara zao bila shida na ameiomba serikali iendelee kuwaboreshea miundombinu ili kuzifikia huduma za kijamii kwa urahisi. 

Bw. Albano Nditi mkazi wa mtaa wa Kiziza ameishukuru serikali kwa kuwaboreshea miundombinu na ameomba waongezewe alama za barabarani na matuta na pia ameomba wananchi wenzake wailinde miundombinu hiyo kwa kuwa wastaarabu na kutotupa takataka kwenye mifereji.










Top News