Na Mwandishi Wetu
RAIS  na Mkurugenzi Mkuu wa Octant Energy, Richard Schmitt, amesema Kampuni hiyo bado ina dhamira ya dhati kuendelea kuwekeza nchini kwa kuzingatia sheria viwango vya kitaalamu na maslahi ya wananchi.

Akizungumza katika banda la Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) kwenye Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara Sabasaba, Schmitt amesema kampuni hiyo inaendelea kutekeleza shughuli zake kwa kushirikiana kwa karibu na PURA pamoja na wadau wengine.

Akiwa katika banda la PURA, Schmitt amepata elimu kuhusu mfumo wa usimamizi wa shughuli za utafutaji, uendelezaji na uzalishaji wa mafuta na gesi asilia nchini pamoja na kuhakikisha rasilimali za Petroli zinazoendelezwa zinazingatia sheria, na uwazi.

Octant Energy ni waendeshaji wa Kitalu cha Uchimbaji Tanga ambao wamefika katika banda la PURA kwenye maonesho ya Sabasaba kama moja ya wadau wa PURA. 



 


*Aipongeza TASAC kutoa gawio la Zaidi ya sh.bilioni 20

Na Mwandishi Wetu
SERIKALI imeihakikishia sekta ya usafiri wa majini kuwa itaendelea kulinda uwekezaji wa vyombo vya majini na mali za wawekezaji ili kuimarisha mazingira salama ya biashara, huku ikiitaka Tanzania Shipping Agencies Corporation (TASAC) kuongeza juhudi katika kuzalisha wataalamu wa sekta ya bahari ili kukidhi mahitaji yanayoongezeka.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile, baada ya kutembelea banda la TASAC katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere.

Kihenzile amesema Serikali imejipanga kuhakikisha wawekezaji wanaowekeza katika meli, boti na vyombo vingine vya majini wanaendelea kufanya shughuli zao kwa usalama, huku ulinzi wa wananchi, wageni na mali zao ukipewa kipaumbele kupitia taasisi husika.

Amesema mazingira hayo salama yataendelea kuongeza imani ya wawekezaji na kuvutia uwekezaji zaidi katika uchumi wa buluu, ambao ni moja ya sekta muhimu zinazochochea ukuaji wa uchumi wa Taifa na kuongeza fursa za ajira kwa Watanzania.

Katika hatua nyingine, Kihenzile ameipongeza TASAC kwa mafanikio yake ya kifedha baada ya kutoa gawio la Shilingi bilioni 20.45, sawa na asilimia 15 ya mapato ghafi ya shirika kwa mwaka wa fedha 2025/26, ambalo lilikabidhiwa kwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Amesema kiwango hicho cha gawio kinaonyesha shirika linafanya kazi kwa ufanisi na kuwataka viongozi na watumishi wake kuendelea kusimamia majukumu yao kwa weledi na uwajibikaji ili kuongeza mchango wa taasisi hiyo katika uchumi wa Taifa.

Akizungumzia ukuaji wa sekta ya usafiri wa majini, Kihenzile amesema ongezeko kubwa la biashara katika bandari za Tanzania limeongeza mahitaji ya wataalamu wa sekta ya bahari, akibainisha kuwa kiwango cha mizigo kilichokuwa kinatarajiwa kufikiwa mwaka 2030 kilifikiwa mapema mwaka 2022 kutokana na uongozi madhubuti, kuimarika kwa diplomasia ya uchumi na ushiriki wa sekta binafsi.

Amesema ukuaji huo unamaanisha kuwa kutahitajika idadi kubwa zaidi ya manahodha, mabaharia, wasaidizi wa mabaharia pamoja na wataalamu wengine wa usafiri wa majini ili kuhudumia shughuli zinazozidi kupanuka.

Kutokana na hali hiyo, ameihimiza TASAC kutotekeleza jukumu la udhibiti pekee, bali kushirikiana na Serikali kuweka mikakati madhubuti ya kuzalisha wataalamu wa kutosha watakaoweza kukidhi mahitaji ya sekta ya bahari inayokua kwa kasi.

Aidha, amewapongeza watumishi wa TASAC kwa uadilifu na weledi wanaouonyesha katika utekelezaji wa majukumu yao, akiwataka kuendelea kufanya kazi kwa uzalendo ili kuhakikisha sekta ya bahari inatoa manufaa makubwa kwa Watanzania na kuchangia maendeleo endelevu ya Taifa.





Mkuu wa Sehemu ya Sheria wa PPAA, Bi. Agnes Sayi akizungumza na waandishi wa Habari kwa niaba ya Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando katika banda la PPAA lililopo ndani ya banda la Wizara ya Fedha kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) yanayoendelea Jijini Dar es Salaam.

*Yaiwezesha Serikali kupata thamani halisi ya fedha
*Wadau ununuzi wa umma 2,600 wafikiwa mafunzo matumizi ya moduli

Na Mwandishi wetu
MAMLAKA ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imefanikiwa kushughulikia rufaa 58 kati ya rufaa 60 zilizowasilishwa katika mwaka wa fedha 2025/26 na kuzitolea uamuzi kwa wakati na kuiwezesha Serikali kupata thamani halisi ya Fedha.

Takwimu hizo zimetolewa na Mkuu wa Sehemu ya Sheria wa PPAA, Bi. Agnes Sayi kwa niaba ya Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando katika banda la PPAA lililopo ndani ya banda la Wizara ya Fedha kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) yanayoendelea Jijini Dar es Salaam.

“Katika mwaka wa fedha 2025/26 PPAA ilipokea rufaa takriban 60 na kushughulikia rufaa 58 kati ya 60 zilizowasilishwa na kuzitolea uamuzi kwa wakati, rufaa mbili zilizosalia zimefanyiwa kazi katika mwaka huu wa fedha,” amesema Bi. Sayi

Aidha, Bi. Sayi ameongeza kuwa baada ya Serikali kuweka sharti la lazima kuwa ununuzi wa Umma kufanyika kwa njia ya Kieletroniki, PPAA kwa kushirikiana na Mamlaka ya Udhibiti Ununuzi wa Umma (PPRA) ilijenga Moduli ya Kupokea na Kushughulikia Malalamiko na Rufaa katika Mfumo wa NeST, na moduli hiyo imeanza kutumika tangu mwezi Februari 2025.

“Ili kuwawezesha wadau wa Ununuzi wa Umma kutumia Moduli hiyo, PPAA imefanikiwa kutoa mafunzo ya matumizi ya Moduli ya Kupokea na Kushughulikia Malalamiko na Rufaa katika mfumo wa NeST kwa wadau wa ununuzi wa umma 2,600 nchini,” amesema Bi. Sayi na kuongeza kuwa mafunzo hayo yaliwahusisha wazabuni takriban 1,907 pamoja na watumishi wa umma 705.

Bi. Sayi ameongeza kuwa PPAA katika maonesho ya Sabasaba inatoa elimu juu ya uwasilishaji na ushughulikiaji wa malalamiko na rufaa zinazotokana na mchakato wa ununuzi wa umma, juu ya rufaa zinazotokana na kufungiwa kushiriki katika michakato ya ununuzi wa umma pamoja na juu ya malalamiko yanayotokana na kushindwa kwa Afisa Masuuli kutoa uamuzi ndani ya muda uliowekwa.

Maeneo mengine yanayotolewa elimu ni kuhusu malalamiko baada ya mkataba wa ununuzi kuanza kutekelezwa, uamuzi juu ya maombi ya kuongezewa muda wa kuwasilisha rufaa nje ya muda uliowekwa, uamuzi juu ya maombi ya utekelezaji wa amri ya Mamlaka ya Rufani, uamuzi juu ya maombi ya kufuta uamuzi uliotolewa bila kusikiliza upande mwingine na uamuzi juu ya maombi ya kurejesha rufaa.

Maonesho ya Sabasaba kwa mwaka 2026 yanaongozwa na kaulimbiu: Maonesho ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba, Fahari ya Tanzania.
Na Mwandishi Wetu

WANANCHI kutoka maeneo mbalimbali nchini wameendelea kujitokeza kwa wingi kutembelea banda la Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) katika Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, kwa lengo la kupata elimu kuhusu usalama, ubora na matumizi sahihi ya dawa, vifaa tiba na bidhaa nyingine za afya.

Katika banda hilo, wataalamu wa TMDA wamekuwa wakitoa elimu kwa wananchi kuhusu namna ya kutambua dawa zilizosajiliwa na mamlaka hiyo, matumizi sahihi ya dawa, pamoja na umuhimu wa kununua dawa na bidhaa nyingine za afya kutoka kwenye maduka na vituo vilivyoidhinishwa ili kujikinga na bidhaa bandia au zisizo na ubora.

Aidha, wananchi wamepata fursa ya kuelezwa majukumu ya TMDA katika kusimamia ubora, usalama na ufanisi wa dawa, vifaa tiba na bidhaa nyingine za afya, sambamba na hatua zinazochukuliwa dhidi ya wanaojihusisha na usambazaji wa bidhaa zisizokidhi viwango.

Baadhi ya wananchi waliotembelea banda hilo wamesema elimu wanayoipata imewasaidia kuongeza uelewa kuhusu matumizi salama ya dawa na umuhimu wa kuhakiki bidhaa za afya kabla ya kuzitumia.

Wamesema maonesho hayo yamekuwa jukwaa muhimu la kuwafikia wataalamu wa TMDA na kupata majibu ya maswali mbalimbali yanayohusu matumizi ya dawa na bidhaa za afya, jambo linalochangia kuimarisha ulinzi wa afya za wananchi.

Kutokana na mwitikio huo, wananchi wamewahimiza Watanzania wengine kutumia fursa ya Maonesho ya Sabasaba kutembelea banda la TMDA ili kupata elimu itakayowasaidia kufanya maamuzi sahihi kuhusu matumizi ya dawa na bidhaa nyingine za afya, hatua ambayo itachangia kujenga jamii yenye afya na kuepuka madhara yanayoweza kusababishwa na matumizi ya bidhaa zisizo salama.




Na Mwandishi Wetu
KAMPUNI ya Yas Tanzania kwa kushirikiana na ZTE imezindua mpango maalumu wa kuwawezesha Watanzania kumiliki rauta za intaneti ya 5G kwa mfumo wa malipo ya awamu, hatua inayolenga kuongeza upatikanaji wa huduma ya intaneti ya kasi kwa wafanyabiashara, kaya na taasisi mbalimbali nchini.

Mpango huo ulizinduliwa katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba), ambapo wateja watapata fursa ya kumiliki rauta ya ZTE 5G kwa kulipa kiasi cha awali cha Sh80,000 na kisha Sh80,000 kila mwezi kwa kipindi cha miezi 12. Kila malipo ya mwezi yataambatana na kifurushi cha intaneti isiyo na kikomo chenye kasi ya Mbps 10.

Uzinduzi huo unakuja wakati Tanzania ikiendelea kushuhudia ukuaji wa uchumi wa kidijitali, huku matumizi ya malipo ya kidijitali yakiongezeka, huduma nyingi za Serikali zikihamia mtandaoni na mahitaji ya intaneti ya uhakika kwa ajili ya elimu, biashara na kazi yakiendelea kuongezeka.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Meneja wa Mauzo ya Vifaa vya Intaneti wa Yas Tanzania, Imelda Edward, alisema ushirikiano huo unalenga kuondoa kikwazo cha gharama ambacho kwa muda mrefu kimewazuia Watanzania wengi kupata huduma bora za intaneti.

Alisema intaneti ya uhakika si huduma ya mawasiliano pekee, bali ni nyenzo muhimu inayofungua fursa za kiuchumi na kijamii kwa wananchi.

"Leo mawasiliano si suala la kuunganishwa na intaneti pekee, bali ni kufungua fursa. Intaneti ya uhakika inawawezesha wajasiriamali kukuza biashara zao, wanafunzi kupata elimu ya kidijitali, wataalamu kufanya kazi kwa ufanisi zaidi na familia kuendelea kuwasiliana. Kupitia ushirikiano wetu na ZTE tunafanya teknolojia ya kizazi kipya ipatikane kwa Watanzania wengi zaidi huku tukichochea ujumuishaji wa huduma za kidijitali nchini," alisema Imelda.

Aliongeza kuwa kwa wafanyabiashara wengi, intaneti imekuwa huduma muhimu kama ilivyo umeme, kwa kuwa ndiyo msingi wa malipo ya kidijitali, biashara mtandaoni, huduma kwa wateja na uendeshaji wa shughuli za kila siku.

"Kila oda inayofanyika mtandaoni, kila malipo ya kidijitali na kila mawasiliano na mteja yanategemea intaneti ya uhakika. Kupitia ushirikiano huu tunawapatia wafanyabiashara suluhisho za kidijitali zitakazowawezesha kuongeza ushindani, ubunifu na kukuza biashara zao," alisisitiza.

Kwa upande wake, mwakilishi wa ZTE, Wen Jiahao, alisema ushirikiano huo unaonesha dhamira ya kampuni hizo mbili ya kupanua upatikanaji wa teknolojia za kisasa za mawasiliano kwa gharama nafuu nchini.

Alisema kwa kuunganisha teknolojia ya 5G ya ZTE na mtandao mpana wa Yas Tanzania, wananchi, familia na wafanyabiashara watanufaika na huduma ya intaneti yenye kasi na uhakika zaidi, hivyo kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kidijitali unaokua kwa kasi.

Ushirikiano huo pia unaonesha dhamira ya Yas Tanzania ya kuendelea kuwekeza katika kuimarisha miundombinu ya kidijitali kupitia upanuzi wa mtandao wa 4G na 5G pamoja na kuanzisha suluhisho mbalimbali zitakazowaunganisha Watanzania wengi zaidi na fursa za uchumi wa kidijitali.

Katika Maonesho ya Sabasaba mwaka huu, wananchi wanaotembelea banda la Yas watapata fursa ya kujionea uwezo wa rauta ya ZTE 5G, kupata maelezo kuhusu mfumo wa malipo wa kuimiliki, huku kifaa hicho kikitarajiwa kupatikana katika maduka yote ya Yas nchini.

Mpango huo unatarajiwa kuchangia utekelezaji wa ajenda ya Taifa ya mageuzi ya kidijitali kwa kuongeza upatikanaji wa intaneti ya kasi kwa gharama nafuu, kuimarisha shughuli za biashara, kuongeza tija katika uchumi na kuwapa Watanzania wengi zaidi fursa ya kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kidijitali.

Na Kassim Nyaki, Ngorongoro.

Mbio za Mwenge wa Uhuru jana tarehe 6 Julai, 2026 zilliwasili Wilaya ya Ngorongoro na kukimbizwa umbali wa kilomita 386 kuzindua miradi mbalimbali ambapo pia umepita katika eneo la hifadhi ya Ngorongoro na kuangazia maajabu saba ya Ngorongoro huku watalii kutoka mataifa mbalimbali wakishuhudia.

Ukiwa katika hifadhi ya Ngorongoro kuelekea Wilaya ya Karatu watalii kutoka mataifa mbalimbali walionyesha bashasha kuona Mwenge ukipita eneo la hifadhi lenye vivutio mbalimbali ambapo tukio hilo linaashiria uwepo wa Amani, umoja na mshikamano wa Kitaifa unaotoa tumaini kwa wageni kufanya shughuli za utalii bila changamoto yoyote.

Mmoja wa wageni kutoka nchini Denmark Ella Wiliams ameeleza kuwa “Tumefurahi kuona Mwenge wa Uhuru ukipita eneo la hifadhi kwa hali ya utulivu na sisi kuwa sehemu ya tukio hili, hii inaashiria kuwa Tanzania pamoja na kuwa na maajabu mengi ya vivutio vya utalii, ni nchi pia yenye amani, umoja na mshkamano unaoshiria Taifa moja lenye watu wanaopendana na kushirikiana”

Kiongozi wa Mwenge wa Uhuru Kitaifa Bw. Wazo Michael Mwang’onda ameeleza kuwa; Ngorongoro ni hifadhi yenye vivutio vingi vya utalii na hadhi za kimataifa ambapo yeye na timu ya wakimbiza Mwenge wa Uhuru kitaifa wanahamasisha amani,umoja na mshkamano wa kitaifa ili kwa pamoja kuletea maendeleo kupitia fedha za kigeni zinazochangiwa na idadi kubwa ya watalii wanaotembelea hifadhi za Ngorongoro na maeneo mengine ya nchi.

Watumishi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro wakiongozwa na Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi anayesimamia Idara ya Wanyamapori na Utafiti Vicktoria Shayo, wameshiriki mbio kupokea Mwenge wa Uhuru katika Wilaya ya Ngorongoro na kuukabidhi leo tarehe 7 Julai, 2026 katika Wilaya ya Karatu.








-Makubaliano yanalenga kuongeza uwazi, ufanisi na upatikanaji wa huduma za kifedha kwa vyama vya ushirika kupitia teknolojia.

Dodoma, Julai 5, 2026 – Mamilioni ya wakulima nchini wanatarajiwa kunufaika na huduma za kifedha kidijitali kufuatia muendelezo wa makubaliano ya ushirikiano kati ya kampuni ya Mixx na Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC).

Makubaliano hayo yanalenga kuboresha usimamizi wa fedha kwa vyama vya ushirika, kuongeza uwazi na uwajibikaji, pamoja na kurahisisha huduma kwa wanachama.

Akizungumza wakati wa hafla ya utiaji saini jijini Dodoma, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo anayesimamia Maendeleo ya Mazao na Usalama wa Chakula, Prof. Peter Msoffe, alisema Biashara zinazopita kwenye vyama vya Ushirika inaribia sh. trilioni 5-7 ambazo zinaingia kwenye uchumi wa nchi na kufanya vyama vya ushirika kuwa moja ya taasisi muhimu katika kuchochea uchumi wa nchi.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Biashara wa Mixx, Ndugu James Sumari, alisema ushirikiano huo utasaidia kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za kifedha kwa wakulima.

"Tunataka vyama vya ushirika viweze kusimamia fedha zao kwa uwazi na kuwafikishia wanachama huduma za kifedha kwa urahisi zaidi. Hii itasaidia kuongeza tija na kuchochea maendeleo ya uchumi wa wananchi," alisema Sumari.

Kupitia mfumo wa Mixx Kikoba, vyama vya ushirika vitaweza kusimamia michango, kufanya malipo, kununua hisa, kupokea gawio na kuomba mikopo kwa njia ya simu za mkononi.

Bwana Sumari aliongeza kuwa, mpaka sasa kupitia jukwaa la Mixx Kilimo, zaidi ya wakulima 300,000 tayari wamefikiwa na huduma za kifedha, huku zaidi ya shilingi bilioni 700 zikiwa zimepitishwa katika sekta ya kilimo katika kipindi cha miaka sita iliyopita.

Naye, Mrajis wa Vyama vya Ushirika na Mtendaji Mkuu wa TCDC, Dkt. Benson Ndiege, alisema matumizi ya teknolojia ni muhimu katika kuboresha sekta ya ushirika.

Serikali inaendelea kuhimiza matumizi ya teknolojia ili kuongeza uwazi na ufanisi katika vyama vya ushirika. Ushirikiano huu utasaidia kuwajengea uwezo viongozi na wanachama kupata huduma bora za kifedha," alisema Dkt. Ndiege.

Makubaliano hayo yanatarajiwa kuongeza matumizi ya huduma rasmi za kifedha kwa wakulima na kuimarisha mchango wa sekta ya ushirika katika uchumi wa Taifa.
Msajili wa Vyama vya Ushirika na Mtendaji Mkuu wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC), Dk. Benson Ndiege (kushoto), akibadilishana hati za makubaliano na Mkurugenzi wa Biashara wa Mixx, Bw. James Sumari, baada ya kuendeleza ushirikiano kati ya Mixx na TCDC wakati wa hafla iliyofanyika jijini Dodoma hivi karibuni. Ushirikiano huo unalenga kuimarisha huduma za kifedha kidijitali kwa vyama vya ushirika, kuongeza uwazi, ufanisi na upatikanaji wa huduma za kifedha kwa mamilioni ya wakulima nchini kupitia matumizi ya teknolojia.


WANANCHI wa kijiji cha Ng'ongo kata ya Mtowisa wilayani Sumbawanga wameiomba serikali kuwajengea nyumba watumishi wa Afya na kuongeza wahudumu katika Zahanati ya kijiji hicho huku Zahanati hiyo ikiwa na wahudumu wawili wote wakiwa ni wauguzi hali inayohatarisha Afya za wakazi wa eneo hilo.

Akijibu ombi hilo kwa wananchi Waziri wa katiba na sheria Juma Homera aliwahakikishia wakazi wa eneo hilo kuwa changamoto hiyo itakwenda kutatuliwa kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo pamoja na wananchi huku waziri huyo akichangia mifuko 100 ya saruji ili kuanza kwa ujenzi wa nyumba ya watumishi wa Afya na kuimarisha huduma za matibabu katika Zahanati hiyo.

Waziri wa katiba na sheria Juma Homera amefungua Zahanati ya kijiji cha Ng'ongo iliyogharim Milioni 120 ikiwa Zahanati hiyo ilianza kujengwa kwa nguvu za wananchi kwa milioni 20 huku serikali ikikamilisha ujenzi huo kwa sh. milioni 100.





Jane Mwakyoma - Rukwa.

SERIKALI Imewaomba wakulima mkoani Rukwa kuwa na subra ya upandaji wa bei ya mahindi  wakati serikali inapolifanyia kazi suala la bei za mahindi nchini.

Akitoa ufafanuzi huo baada ya mkuu wa wilaya ya Sumbawanga akimwakilisha mkuu wa mkoa wa Rukwa Nyakia Chirukile baada ya kumuomba Waziri wa katiba na sheria kuhusu serikali kupandisha bei ya mahindi mkoani humo baada ya kukagua ujenzi wa stendi ya mabasi Laela.

Homera amesema serikali ya Dk. Samia Suluhu Hassan inashughulikia changamoto za wananchi katika kuhakikisha wananchi wake wanaondokana na changamoto ya bei ndogo ya mahindi ili kuwainua wakulima kiuchumi.

" Niseme suala la bei ya mazao kila sehemu hii changamoto ipo, ukienda mimi jimbo langu ni Namtumbo, pale wanalima mahindi miongoni mwa mikoa inayolima mahindi ni Ruvuma ,Rukwa, Katavi nadhani na Iringa pia lakini bei ya mahindi huku kwetu imeshuka kwa kiwango kikubwa lakini ndugu zangu niwatoe mashaka hili jambo serikali ya CCM inayoongozwa na Dk. Samia Suluhu Hassan chini ya waziri wa kilimo Daniel Chongoro, inalifahamu kwaiyo tuendelee kuwa na subra kidogo serikali inapolifanyia kazi " amesema Homera.

Pia Homera amesema suala la mbolea serikali ya awamu ya sita inalishughulikia suala hilo na kuwataka wananchi kuendelea kusubili huku serikali ikisisitiza wakulima kuendelea kujiandikisha ili kupata mbolea za ruzuku.

Aidha amewataka wananchi kutoa ushirikiano kwa vyombo vya sheria kwa watu wanaotaka kuvuruga amani katika nchi.

Pia amesema wananchi wasikubali kudanganywa kwasababu ya maslahi ya watu wachache na badala yake wahakikishe wanailinda amani ya nchi kwa wivu mkubwa ili kuendelea na shughuli zao za kiuchumi kwa amani na utulivu.

Waziri wa katiba na sheria Juma Homera yupo mkoani Rukwa kwa ziara ya siku nne kwa lengo la kukagua, kutembelea,kuweka mawe ya msingi,kufungua miradi ya maendeleo na kusikiliza kero za wananchi.



Jane Mwakyoma,Rukwa.

WAZIRI wa katiba na sheria Juma Homera ameagiza Taasisi ya kupambana na rushwa (TAKUKURU) mkoani Rukwa kuchunguza madai ya wahudumu wa Afya wa hospital ya wilaya Mtowisa wilayani Sumbawanga wakidaiwa kuwatoza wananchi shilingi 40,000 kwa watoto chini ya miaka mitano wanapopatiwa matibabu na waliojifungua watoto wa kiume hutozwa shilingi elfu kumi ikiwa ni kinyume cha sheria na matakwa ya serikali.

Akitoa maagizo hayo mara baada ya wananchi kutoa kero zao katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika kijiji cha Mtowisa kata ya Mtowisa wilayani Sumbawanga Homera alisema serikali imeweka mipango ya wajawazito na watoto chini ya miaka mitano kutibiwa bure katika hospitali za serikali na kuwa endapo kutakuwa na wahudumu wa Afya watakao kwenda kinyume na mtakwa ya serikali watachukuliwa hatua za kisheria na kinidhamu.

"Kwanza inasikitisha sana huwezi kuwatoza pesa wamama wajawazito akijfungua mtoto wa kiume unamtoza pesa, akijfungua mtoto wa kike unamtoza pesa,jambo hili Taasisi ya kupambana na rushwa waanze kufanyia kazi mara moja ikiwemo na kufanya uchunguzi kwa kina katika hospitali ya wilaya na kuanza kuwabaini wahudumu wa Afya ambao siyo wema kwa watanzania tukianza kuyafumbia macho haya kesho wataiba hadi watoto watawapa watoto watu wengine."

"Sasa lazima tuhakikishe kwamba kama mtu atatozwa sh.10000 lazima mtumishi huyo achukuliwe hatua ,ofisi ya mkuu wa wilaya mpo hapa na TAKUKURU hakikisheni tarehe ya kufanya majumuisho tupate na kama mmetoa katazo tupate taarifa hiyo "amesisitiza Homera.

Aidha amepiga marufuku kwa watumishi wa Afya kuwatoza fedha wamama wajawazito na watoto chini ya miaka mitano kuwa serikali ya awamu ya sita imeagiza kundi hilo kutibiwa bure katika hospitali za serikali.

"kwanza Ni marufuku kuwatoza wananchi fedha sh.40000 au elifu kumi, serikali imeagiza wamama wajawazito na watoto chini ya miaka mitano kutibiwa bure,kuna baadhi ya watumishi wasiyo waadilifu wanaichonganisha serikali na wananchi hatutakubali mtumishi atuchonganishe" alisisitiza Homera.

Aidha amewataka viongozi wa sekta mbalimbli nchini kujijengea mazoea ya kusikiliza kero na changamoto za wananchi na kuzitatua ili wananchi waendelee kuwa na imani na serikali yao.

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Sumbawanga Nyakia Chirukile amekili kuwepo kwa changamoto ya wajawazito wakati wa kujifungua na watoto chini ya miaka mitano kutibiwa kwa kutozwa fedha ikiwa ni kinyume na taratibu zilizowekwa.

Amesema alipigiwa simu na baadhi ya wananchi kueleza kero hiyo ambapo alimwagiza mganga mkuu wa wilaya kulifanyia kazi suala hilo ikiwemo kupatikana kwa kipimo cha tyaphodi ambacho mpaka sasa hospitali hiyo haina kipimo hicho na kuwa wananchi wamekuwa wakielekezwa kutozwa kiasi kikubwa cha pesa wakidai kipimo kilichopo siyo mali ya serikali bali ni mali ya mtu binafsi.





Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Mauritius, Kamishna wa Polisi (CP) Suzan Kaganda, mwenye makazi yake ya kikazi Jijini Harare, Zimbabwe, amewasilisha Hati za Utambulisho kwa Rais wa Jamhuri ya Mauritius, Mhe. Dharambeer Gokhool, katika hafla iliyofanyika Julai 6, 2026, Ikulu ya Serikali iliyopo Reduit, Mauritius.

Baada ya kuwasilisha hati hizo, Balozi Kaganda alifanya mazungumzo na Mheshimiwa Rais Gokhool, ambaye alimpongeza kwa uteuzi wake na kumkaribisha rasmi katika eneo lake la uwakilishi, huku Rais huyo pia akimhakikishia ushirikiano na Serikali ya Mauritius katika kipindi chote cha utekelezaji wa majukumu yake ya kidiplomasia.

Kwa upande wake, Balozi Kaganda alishukuru kwa mapokezi mazuri aliyopatiwa na kuahidi kuendeleza ushirikiano wa karibu na Serikali ya Mauritius katika kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Mauritius ambapo aliweka wazi kuwa dhamira yake ni kuendeleza ushirikiano katika sekta za biashara, uwekezaji, utalii na Uchumi wa Buluu kwa manufaa ya wananchi na maendeleo ya nchi hizo mbili.

Balozi (CP) Kaganda pia anaiwakilisha Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Zimbabwe, akiwa na makazi ya kikazi jijini Harare.






📍NIRC: DODOMA

Tume ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC) imeanza kuweka mikakati ya jinsi ya kusafirisha mitambo yake mikubwa ya kuchimba visima virefu kwenda maeneo mbalimbali nchini, hususani yale yenye changamoto kubwa ya upatikanaji wa maji chini ya ardhi, mara baada ya kukamilisha kazi katika shamba la Chinangali.

Mkurugenzi Mkuu wa NIRC, Raymond Mndolwa, ametoa agizo hilo kwa Idara ya Mitambo, ya Tume hiyo kutathmini namna bora ya kusafirisha mitambo hiyo bila kuathiri miundombinu ya barabara kutokana na uzito wake mkubwa.

“Tuone namna bora kwa Idara husika kushauri kama tunaweza kusafirisha mitambo hii nusu nusu (kwa kuifungua) kutokana na uzito wake, ili isiathiri barabara zetu inapokwenda mikoa tofauti,” amesisitiza Mndolwa.

Agizo hilo amelitoa wakati wa ziara yake katika shamba la vijana la mradi wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) lililopo Chinangali mkoani Dodoma.

Ziara hiyo ililenga kukagua maendeleo ya ujenzi wa barabara za ndani, mabwawa,uchimbaji wa visima na uwekaji wa miundombinu ya Umwagiliaji katika mashamba hayo,inayotekelezwa na Tume hiyo.

Katika ziara hiyo, Mndolwa alikagua mtambo huo wa kisasa wenye uwezo wa kuchimba visima virefu hadi mita 1,800 chini ya ardhi, ambao kwa sasa upo Chinangali kwa ajili ya kuchimba visima viwili vya mwisho. Visima hivyo vitakamilisha jumla ya visima 40 vinavyochimbwa na NIRC shambani hapo, sambamba na mabwawa matatu ambapo mawili tayari yamekamilika ili kuongeza kasi ya upatikanaji wa maji.

Mndolwa aliambata na wataalamu mbalimbali akiwemo Mkurugenzi wa Idara ya Uendelezaji Miundombinu Mhandisi Leopard Runji, Mhandisi wa Mkoa wa Dodoma Oswald Urassa na Muendesha Mitambo hiyo ya Visima virefu Mosses Mkude. 






Top News