Huu ni wakati wa kuunganisha nguvu, hekima na uzoefu wetu kwa manufaa ya taifa letu. Muda ni sasa. Tunawahimiza wadau wote kujitokeza kwa wingi na kushiriki kikamilifu katika mkutano huu muhimu.Imetolewa na: Simba A. Simba Mwenyekiti Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira Tanzania
Tarehe: 24 Machi 2026
Na. OWM- KAM
Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Rahma Kisuo amewataka wataalamu na wadau wa Ustawi wa Jamii kufanya kazi kwa weledi, uadilifu katika utendaji kazi hususani kwa watoto na wananchi wanyonge.
Ameyasema hayo Machi 24, 2026 Jijini Dodoma wakati alipofungua Kongamano na Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Wataalamu wa Ustawi wa Jamii Tanzania (TASWO) huku akiwasisitiza wataalam hao kutumia teknolojia (mifumo ya Kielektroniki) katika utendaji kazi ili kurahisisha ukusanyaji wa taarifa mbalimbali.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama wa wataalamu wa Ustawi wa Jamii (TASWO) Dkt. Mariana Makuu akizungumza kwenye kikao hicho alisema kongamano limelenga kuwakutanisha wanataaluma wa huduma za ustawi wa jamii, watunga sera ,wanafunzi na wakufunzi kutoka vyuo vinavyotoa taaluma za ustawi wa jamii ili kujadili kwa pamoja maswala ya kitaalamu kwa lengo kuu la kuboresha elimu ,sera na huduma za utawi wa nchi.

Na Mwandishi Wetu.
Katika hatua ya kuondoa mzigo wa gharama za matibabu kwa wananchi, Serikali imezindua utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Bima ya Afya kwa Wote, utakaowezesha familia ya watu sita kupata huduma za afya 372 kwa gharama ya Sh 150,000 kwa mwaka.
Kwa mujibu wa Mratibu wa Elimu kwa Umma wa Mpango wa Taifa wa Bima ya Afya kwa Wote, Said Makora, mpango huo ni sehemu ya mkakati wa Serikali kuhakikisha huduma za afya zinawafikia wananchi wote bila kujali uwezo wao wa kifedha.
Amesema kupitia mpango huo, huduma zitakazotolewa zinajumuisha uchunguzi wa maabara, radiolojia, dawa na vifaa tiba pamoja na upasuaji mdogo na mkubwa, kuanzia ngazi ya zahanati hadi hospitali za rufaa za taifa.
Makora alibainisha kuwa Serikali kupitia Wizara ya Fedha imeweka vyanzo maalum vya mapato vitakavyokusanya takribani Sh bilioni 201.9 katika mwaka wa fedha 2025/2026 ili kugharamia wananchi wasio na uwezo, huku zaidi ya Sh bilioni 48.2 zikiwa tayari zimekusanywa katika robo ya kwanza ambazo zitakazonufaisha kaya laki 276.
Aliongeza kuwa mpango huo pia unalenga kupunguza vifo vinavyoweza kuzuilika kwa kuimarisha huduma za afya ya mama na mtoto pamoja na kudhibiti magonjwa yanayoongoza kuathiri wananchi kama malaria, kifua kikuu na UKIMWI.
Kuhusu walengwa wa mpango huo, alisema tayari zaidi ya kaya 931,000 zimetambuliwa kupitia kanzidata ya TASAF, huku Serikali ikilenga kufikia zaidi ya kaya milioni 3.9 zitakazonufaika na mpango huo, gharama zao zikigharamiwa kikamilifu.
“Mpango huu unakwenda kubadili maisha ya wananchi kwa kuhakikisha wanapata huduma za afya kwa wakati bila hofu ya gharama,” alisema Makora.
Utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote unatarajiwa kuongeza usawa katika upatikanaji wa huduma za afya, kupunguza umasikini unaosababishwa na gharama za matibabu na kuimarisha ustawi wa jamii kwa ujumla.
Akizungumza leo jijini Dar es Salaam katika mahafali ya wahitimu wa mradi huo, Mratibu wa Women Creating Wealth (WCW), Angaja Mwanga amesema kuwa hadi sasa mradi huo umefanikiwa kuwafikia wanawake wajasiriamali zaidi ya 10,000, hatua inayotarajiwa kuchochea ukuaji wa uchumi wao binafsi pamoja na kuwasaidia kufikia masoko mapana zaidi.
Kwa upande wake, mtoa mada wa mradi huo, Fatma Abdallah Kange amesema wanawake wengi katika jamii wanakabiliwa na changamoto za ukosefu wa ujuzi na uzoefu wa kibiashara, hivyo mafunzo yanayotolewa kupitia mradi huo yanalenga kuziba pengo hilo na kuwawezesha kufanya biashara kwa ufanisi.
Nao baadhi ya wahitimu wa mradi huo, akiwemo Asimin Gombo na Mectlida Godfrey, wameeleza kuwa mafunzo waliyopata yamewajengea uwezo mkubwa wa kuendesha na kukuza biashara zao, pamoja na kuwasaidia kutafuta na kupanua masoko.
NA MWANDISHI WETU, CHWAKA
Katika kuboresha sekta ya elimu Mwakilishi wa Jimbo la Chwaka Mhe. Issa Gavu leo Machi 25,2026 amekabidhi vitabu kwa ajili ya kujisomea pamoja na vifaa mbali mbali vya elimu, lengo ikiwa ni kuleta mabadiliko katika kukuza kiwango cha ufaulu kwa wanafunzi wa skuli zote la Jimbo hilo.
Akikabidhi msaada huo Mwakilishi wa Jimbo la Chwaka, Mhe Gavu amebainisha kwamba wameamua kutoa msaada wa vifaaa mbali mbali kwa wanafunzi hao ikiwemo kompyuta mpakato,Printer, vitabu mbali mbali pamoja na mashine ya kuburuzia karatasi (Photocopy mashine) vyote vikiwa vimegharimu kiasi cha shilingi milioni 12,msaada ambao umetolewa kutoka kwa marafiki wema kwa watu wa Jimbo la Chwaka.
"Leo tumejumuika hapa kwa ajili ya kukabidhi vifaa mbali mbali kwa wanafunzi ambao wanasoma katika Jimbo la Chwaka na katika siku ya leo tumekabidhi vifaa mbali mbali ikiwemo vitabu kwa ajili ya kujisomea wanafunzi, Photocopy mashine, pamoja Printer ambavyo vitaweza kuwa ni mkombozi mkubwa kwa wanafunzi kuweza kuongeza kasi ya ufaulu katika masomo yao,"amebainisha Mhe. Gavu.
Aidha katika tukio hilo pia Mhe. Gavu kwa kushirkiana na marafiki zake wa Jimbo hilo pia wametoa msaada wa kugawa mabati katika Skuli ya Mrembo Uroa,Mashine ya kufulia nguo (Washing Machine), tanki la maji na mipira Jendele, pamoja na mafeni na vifaa vya umeme kwa Kituo cha Afya Cheju.
Gavu amesema kwamba wameamua kutoa misaada hiyo katika nyanja mbali mbali ikiwa ni moja ya hatua ya kuimarisha suala la elimu kwa wanafunzi pamoja na kuboresha afya kwa jamii ambayo inawazunguka hasa katika Jimbo la Chwaka na kuwasihi wanafunzi wasome kwa bidii,lengo ikiwa ni kuongeza maarifa ambayo yatawasaidia katika siku za usoni.
Makamu wa Rais amesema hayo, wakati akifungua Kongamano la Kimataifa kuhusu maboresho ya sera ya elimu na mitaala nchini, linalofanyika katika Ukumbi wa Maktaba Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Jijini Dar es Salaam. Ameitaka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kushirikiana na Taasisi za elimu, hususan Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kuendelea kufanya ufuatiliaji na tafiti ili kubaini dosari zozote zinazoweza kukwamisha utekelezaji wa suala hilo ili kubaini na kuibua maeneo yanayohitaji maboresho zaidi kiutendaji.
Makamu wa Rais, amesema suala la utekelezaji wa mabadiliko na maboresho yaliyofanyika kwenye Sera yetu ya Elimu na Mafunzo, na Mitaala kuanzia Elimu ya Awali, Msingi, Sekondari hadi Elimu ya Juu. linataka Watanzania wote kutafsiri vema maono ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan juu ya mfumo wa elimu unaozingatia kutoa ujuzi na maarifa ili kumwezesha mhitimu kumudu mazingira yake, na kumudu ushindani kwenye ulimwengu wa kazi.
Aidha, Makamu wa Rais amesema suala la elimu jumuishi inayozingatia usawa ni miongoni mwa vipaumbele, ambapo Serikali imeweka msisitizo katika uwepo wa vifaa vya kufundishia na kujifunzia pamoja na miundombinu rafiki kwa ajili ya wanafunzi wenye mahitaji maalum. Amesema suala hilo linakwenda sambamba na uandaaji wa walimu wenye ujuzi wa elimu maalum ili kufundisha wanafunzi hao.
Kwa upande wake Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Prof. Adolf Mkenda amesema kongamano hilo la kimataifa kuhusu maboresho ya sera na elimu na mitaala ni fursa nzuri ya ushirikishwaji wa watalaam na wachambuzi kuangalia jinsi ambavyo utekelezaji huo unaendelea.
Amesema kongamano hilo litaangazia zaidi namna bora na ufanisi ya kutekeleza mageuzi ya elimu nchini.
Awali akitoa Taarifa kuhusu Kongamano hilo, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Prof. William Anangisye amesema malengo ya kongamano hilo ni kutafakari na kujenga uelewa wa pamoja miongoni mwa wadau mbalimbali kuhusu sera ya sasa ya elimu na mafunzo na marekebisho ya mitaala na athari zake kwa maendeleo endelevu.
Pia, amesema lengo lingine ni kuibua mijadala ya kitaaluma kuhusu mitaala ya elimu ya msingi, sekondari na elimu ya juu, kutafakari juu ya maendeleo ya kitaaluma na nafasi ya elimu ya ualimu kulingana na maboresho ya sera ya elimu na mafunzo, kubadilishana uzoefu wa kimataifa na kikanda jinsi maboresho ya elimu yanavyoweza kuchangia ukuaji jumuishi na mustakbali wa maendeleo endelevu.
Maboresho yaliyofanywa na serikali kwenye baadhi ya maeneo ya Sera ya Elimu na Mafunzo, yamefanyika ili kuondoa changamoto mbalimbali zilizokuwa zikiikabili elimu ya Tanzania, zikiwemo, kujikita zaidi kwenye elimu ya nadharia badala ya vitendo na pia, kutokuwepo kwa fursa za elimu na mafunzo zinazozingatia mahitaji ya soko la ajira. Vilevile, mapungufu katika njia za ujifunzaji ambazo hazikukidhi hali halisi ya mazingira na maadili ya Kitanzania.
-Ni uwekezaji unaohusisha Kampuni ya Denham ya Marekani.
-Rais Samia apongezwa kufanikisha mradi wa uchimbaji Niobium
-Kiwanda cha kuyeyusha ferroniobium kitakachojengwa Tanzania kitakuwa cha nne duniani
-Waziri Mavunde asema Tanzania kuchangia takriban asilimia 4 ya uzalishaji wa Niobium na uzalishaji wa takriban tani 100,000 kwa mwaka
-Ajira kufikia takriban watu 7,000
MBEYA, Machi 24, 2026 — Tanzania imeingia hatua muhimu ya kuimarisha biashara na Marekani baada ya Serikali na Panda Hill Tanzania Limited kusaini mkataba wa makubaliano ya kuendeleza Mradi wa Niobium wa Panda Hill, hatua inayolenga kuifanya Mbeya kuwa kitovu cha uzalishaji na usindikaji wa madini mkakati.
Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Madini Mheshimiwa Anthony Mavunde alisema mradi huo ni wa uzalishaji wa madini adimu ambayo hayapatikani kila mahali duniani, na kwamba Tanzania inalenga kuchukua nafasi ya kipekee katika soko la kimataifa la niobium kupitia mradi huo. Alisema soko la dunia kwa sasa linatawaliwa na wazalishaji wachache wakubwa, na Panda Hill itaiweka Tanzania kwenye ramani ya wazalishaji wakuu duniani.
Mheshimiwa Mavunde alieleza kuwa mzalishaji mkubwa duniani yupo Brazil na huzalisha takriban asilimia 80 ya mahitaji ya dunia, mzalishaji wa pili naye yupo Brazil na huzalisha takriban asilimia 11, huku Canada ikichangia takriban asilimia 6. Kupitia Panda Hill, alisema Tanzania inalenga kuwa mzalishaji wa nne duniani kwa kuchangia takriban asilimia 4 ya mahitaji ya dunia, na uzalishaji unaolengwa kufikia takriban tani 100,000 kwa mwaka.
Katika kusisitiza mwelekeo wa Serikali, Waziri Mavunde alisema dira ya maendeleo ya 2025-2050 na maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan yanalenga kuhakikisha madini yanaongezewa thamani hapa hapa nchini ili manufaa yawe makubwa kwa wananchi. Alisema Tanzania inaenda zaidi ya uchimbaji wa kawaida kwa kujenga uwezo wa ndani wa kuchakata na kuzalisha bidhaa za viwandani zenye thamani kubwa.
Mradi huo unahusisha niobium, madini ya kimkakati inayotumika kuongeza uimara wa chuma na kutengeneza aloi za utendaji wa juu zinazohitajika kwenye miundombinu mikubwa, miundombinu na matumizi ya teknolojia za kisasa. Waziri Mavunde alitaja pia matumizi katika maeneo ya kisasa kama yanayohusiana na magari ya umeme na injini za ndege, akieleza kuwa hii inaongeza uzito wa mradi katika uchumi wa kisasa wa viwanda.
Kwa upande wa mwekezaji, Dennis Cook, ambaye ni Meneja Mkuu wa Panda Hill Tanzania Limited, alisema kampuni inaingia kwenye hatua mpya ya utekelezaji kwa kushirikiana na Serikali kama mshirika rasmi, baada ya kipindi kirefu cha majadiliano na maandalizi. Alieleza kuwa mradi ulikuwa karibu kuanza ujenzi mwaka 2017 kabla ya mabadiliko ya sheria, na tangu wakati huo kampuni imekuwa ikifanya kazi kwa karibu na Serikali kuhitimisha makubaliano ya msingi ya kuusukuma mradi mbele.
Cook alisema hatua zinazofuata ni kuendelea na taratibu za kupata Leseni Maalum ya Uchimbaji Madini, kusasisha taarifa za upembuzi yakinifu ili kuakisi gharama za sasa za uwekezaji na uendeshaji, kuingiza matumizi ya umeme wa gridi kwenye mpango wa uendeshaji, pamoja na kufanya tathmini ya masoko ya ferroniobium ili kuhakikisha bidhaa inaingia kwa ushindani kwenye soko la dunia, ikiwemo soko la Marekani.
Kwa mujibu wa taarifa za kampuni hiyo, mradi unahusisha ujenzi wa mgodi wa niobium pamoja na kituo cha uchenjuaji na kiwanda cha kuzalisha ferroniobium, bidhaa yenye thamani iliyoongezwa inayohitajika na viwanda vya chuma na uzalishaji wa viwandani. Kampuni imeeleza kuwa bidhaa hiyo inalengwa kuuzwa kwenye masoko ya Afrika, Asia, Ulaya na Marekani, na hivyo kuifanya Tanzania kuwa mshiriki wa moja kwa moja katika minyororo ya ugavi ya viwanda ya thamani ya juu.
Kipengele kinachoifanya Panda Hill kuwa ya kipekee, kwa mujibu wa taarifa za kampuni, ni ujenzi wa kiwanda cha ferroniobium ambacho kitakuwa cha pekee barani Afrika na kitakuwa cha nne kujengwa duniani katika kipindi cha miaka 40 iliyopita. Hili linaipa Tanzania nafasi ya kuingia kwenye kundi dogo la nchi zenye uwezo wa kuzalisha bidhaa hiyo kwa kiwango cha viwandani.
Kwa biashara za ndani na wazabuni wa Tanzania, mradi umebeba fursa kubwa ya muda mrefu. Panda Hill imeeleza kuwa katika maisha ya mradi, thamani ya manunuzi ya ndani inakadiriwa kufikia Dola za Marekani bilioni 1.77, huku asilimia 70 ya manunuzi ya bidhaa na huduma ikilengwa kufanyika ndani ya nchi wakati wa uzalishaji. Hii, kwa maelezo ya wadau, inamaanisha mikataba ya muda mrefu kwa kampuni za Kitanzania katika maeneo ya ujenzi, usafirishaji, matengenezo, huduma za kiufundi, ulinzi, chakula na huduma nyingine muhimu za uendeshaji.
Kuhusu ajira, Waziri Mavunde alisema mradi unatarajiwa kuajiri zaidi ya 1,600 kusaidia ujenzi na kutoa ajira za kudumu takriban 600, huku jumla ya watu watakaonufaika moja kwa moja na wasio wa moja kwa moja ikitarajiwa kufikia takriban 7,000.
Mradi uko katika eneo la Gereza la Kilimo la Songwe, na Waziri Mavunde alieleza kuwa takriban ekari 5,434 za eneo la mradi zipo ndani ya eneo la gereza hilo. Aliongeza kuwa mpango wa utekelezaji unahusisha ujenzi wa gereza jipya la kisasa, akieleza kuwa linalenga kuwa miongoni mwa magereza ya kisasa zaidi katika Afrika Mashariki na Kati.
Waziri Mavunde alisisitiza pia kuwa kurejesha kwa jamii ni sharti, akisema uwajibikaji wa mwekezaji kwa jamii na miradi ya kijamii ni sehemu ya lazima ya uendeshaji wa mradi, sambamba na mapato ya Serikali kupitia kodi, tozo na ushuru mbalimbali.
Kwa upande wa ushiriki wa Serikali, ilielezwa kuwa Tanzania itakuwa na umiliki wa hisa asilimia 16 kupitia mfumo wa free carried interest, unaolenga kuimarisha ushiriki wa Taifa katika maamuzi ya kimkakati na faida za mradi. Katika hatua ya utiaji saini, Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali Samwel M. Maneno alisaini Framework Agreement kwa niaba ya Serikali, huku Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na Msajili wa Hazina Nehemiah Mchechu wakisaini Shareholder Agreement na wawekezaji, kukamilisha muundo wa ushiriki wa Serikali na mfumo wa usimamizi wa mradi.










BENKI ya NMB na Chuo Kikuu cha Tumaini Dar es Salaam (DarTU – zamani TUDARCo), wamesaini Makubaliano ya Ushirikiano (MoU) wa Kimkakati, wenye lengo la kujenga mfumo rasmi wa uandaaji vijana na kuwajengea maarifa ya kitaaluma, ujuzi wa vitendo na uzoefu wa kukabiliana ushindani wa Soko la Ajira.
Ushirikiano huo wa miaka mitatu, unakwenda kuweka msingi imara wa kuunganisha nguvu kati ya Sekta ya Fedha na Taasisi ya Elimu ya Juu katika kujenga taifa kupitia maendeleo ya rasilimali watu wenye ujuzi, maarifa na uwezo unaohitajika katika uchumi wa kisasa.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo iliyofanyika leo Jumatano ya Machi 25 jijini Dar es Salaam, Afisa Mkuu wa Rasilimali Watu wa NMB, Emmanuel Akonaay, alisema Sekta ya Elimu ni miongoni wa vipaumbele vya benki yake katika mkakati endelevu wa Uwezeshaji kwa Jamii (CSI).
“Elimu ni chachu ya maendeleo na mafanikio ya jamii yoyote. Sisis NMB tunaamini kupitia elimu, tunawaandaa vijana wetu kuwa viongozi bora na mahiri wa kesho, wenye uwezo wa kukabiliana na changamoto za maisha na kuchangia katika maendeleo ya nchi yetu.
“NMB tunayo dhamira ya kusaidia maendeleo ya Sekta ya Rasilimali Watu nchini na hatutosita kuendelea kutumia kila nafasi tutakayopata katika kuunga mkono juhudi za kuboresha maendeleo ya taaluma kupitia fursa za mafunzo kwa vitendo,” alisisitiza Akonaay.
Alifafanua kuwa, kupitia ushirikiano huo benki yake inakusudia kupunguza pengo lililopo kati ya elimu inayotolewa vyuoni na mahitaji halisi ya Soko la Ajira, wakiamini kwamba kwa kufanya hivyo, wanasaidia kujenga kizazi cha wataalamu waliobobea, wabunifu, na wenye uwezo wa kushindana kikamilifu.
“Makubaliano haya na DarTU yanaenda kugusa moja kwa moja katika maeneo yafuatayo: Ukuzaji wa Vipaji na Ujuzi, ambako NMB na DarTU tutashirikana katika kutambua na kuendeleza vipaji kupitia mafunzo kwa vitendo kwa wanafunzi wanaofanya vizuri.
“Pia, wafanyakazi wa NMB watapata nafasi za kujiunga na Kozi za Muda Mfupi na Programu za Maendeleo ya Kitaalamu za DarTU, hivyo basi kujiongezea ujuzi muhimu na kukuza utamaduni endelevu wa kujifunza,” aliongeza Akonaay mbele ya Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Prof. Burton Mwamila.
Aidha, aliyataja maeneo mengine yatakayoguswa na MoU hiyo kuwa ni pamoja na ushirikiano wa pamoja baina ya NMB na DarTU katika maeneo ya kufanya utafiti pamoja na kushiriki shughuli za jamii, sambamba na ufanikishaji wa maonesho (Career Fairs), na programu za kujenga uwezo na ujuzi kwa wanafunzi na wafanyakazi.
Aidha, alibainisha ya kwamba ushirikiano huo unaakisi dhamira ya dhati ya taasisi hizo mbili kuwa mstari wa mbele katika uwekezaji wa kimkakati na kuendeleza rasilimali watu, huku ukiwa pia ni uthibitisho wa azma yao ya pamoja ya kuhakikisha Tanzania inakuwa na nguvu kazi bora.
Akonaay aliongeza ya kwamba wanajivunia ushirikiano huo alioutaja kuwa unaendana vyema na vipaumbele vya kimkakati vya benki yake, pamoja na Maono ya Dira ya Taifa 2050, yanayoangazia umuhimu wa nguvu kazi yenye ujuzi na ubunifu mahali pa kazi.
Kwa upande wake, Makamu Mkuu wa DarTU, Profesa Mwamila aliishukuru NMB na kwamba wanajivunia ushirikiano huo, ambao licha ya mkataba wao kuwa wa miaka mitatu, utakuwa ukifanyiwa tathmini kila baada ya mwaka mmoja na upo uwezekano mkubwa wa kuurefusha pindi utakapofikia ukomo.
Alisema kupitia makubaliano hayo, DarTU itatoa huduma ya mafunzo na ushauri kwa NMB kama taassisi pamoja na wafanyakazi wake, huku yakiwawezesha wanafunzi wa DarTU kufanya mafunzo kwa vitendo katika benki hiyo, fursa ambayo itawasaidia kulijua soko kabla ya kuhitimu masomo yao.
“Miongoni mwa changamoto zetu zilikuwa ni pamoja na wanafunzi wetu kukosa taasisi za kufanyia mafunzo kwa vitendo ama niite mazoezi, lakini pia kumaliza masomo na kupata shahada zao, wakiwa hawajapata fursa za kujitolea kabla ya kuingia katika Soko la Ajira, changamoto zinazoenda kwisha kwa mkataba huu.
“Lakini pia, sisi hapa tuna shule zinazofundisha nyanja mbalimbali ikiwemo Sheria, Biashara na hata Elimu ya Kidigitali na Huduma za Ushauri, ambako pia tuna Kitengo Maalumu cha Usalama wa Mtandao (cyber security), kinachosaidia sana kutoa elimu ya kuzuia mifumo ya kiusalama ya taasisi kuingiliwa.
“Aidha, sisi kwa sababu ni Chuo cha Elimu ya Juu, tunafuatilia sana maendeleo ya elimu na teknolojia katika maeneo yote na tuko mbele ya muda kuliko taasisi mbalimbali nchini,” alibainish Profesa Mwamila wakati wa hafla hiyo na kuongeza:
“DarTU tunao wajibu mkubwa wa kusaidia kile tulichonacho kuwashirikisha Watanzania zikiwemo taasisi, kwahiyo makubalinao haya yatatuwezesha kuendesha mafunzo ambayo yatawawezesha wafanyakazi wa NMB kwenda na wakati katika maeneo yao ya kazi.”
Afisa Mkuu Rasilimali Watu wa Benki ya NMB, Bw. Emmanuel Akonaay (kushoto) pamoja na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Tumaini (DarTu), Prof. Burton Mwamila (kulia) wakibadilishana hati za makubaliano ya ushirikiano kati ya taasisi hizo leo jijini Dar es Salaam. Kwa makubaliano hayo wanafunzi kutoka Chuo Kikuu cha Tumaini watapata fursa ya kujifunza kwa vitendo NMB kabla ya kuingia kwenye ajira na wafanyakazi wa NMB watapata fursa ya kuongeza elimu ya masuala ya sekya ya kibenki kwenye chuo hicho.Afisa Mkuu Rasilimali Watu wa Benki ya NMB, Bw. Emmanuel Akonaay (wa pili kushoto) pamoja na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Tumaini (DarTu), Prof. Burton Mwamila (wa tatu kulia) wakisaini makubaliano ya ushirikiano kati ya taasisi hizo leo jijini Dar es Salaam, wa kwanza kulia ni Meneja wa Kanda wa NMB, Bw. Seka Urio na mwanasheria wa NMB, Bw. Fred Abacha (wa kwanza kushoto) na mwanasheria wa DarTu, Bw. Amani Mwakyoma ambapo pamoja na mambo mengine wanafunzi kutoka Chuo Kikuu cha Tumaini watapata fursa ya kujifunza kwa vitendo NMB kabla ya kuingia kwenye ajira na wafanyakazi wa NMB watapata fursa ya kuongeza elimu ya masuala ya sekya ya kibenki kwenye chuo hicho.
.jpeg)
.jpeg)

Mradi wa Ujenzi wa Daraja la Zege la Gagi linalojengwa Kata ya Ndembezi Manispaa ya Shinyanga kupitia Mfuko wa Dharura (CERC) limeondoa adha ya usafiri iliyokuwa inawakabili kwa muda mrefu wananchi wa Kata hiyo na maeneo ya jirani.
Daraja hilo lenye urefu wa mita 11.2 na upana mita 8.2 linajengwa kwenye barabara ya Gagi ambalo linaunganisha Kata za Ndembezi na Ngokolo katika Manispaa hiyo.
Akizungumza kwenye mahojiano maalum katika ziara ya kutembelea mradi huo, Diwani wa Kata ya Ndembezi na Naibu Meya wa Manispaa ya Shinyanga Mhe. Upendo John Sawa amesema kukosekana kwa daraja hilo ni kilio cha muda mrefu kwa wananchi wa Kata hiyo kutokana na ugumu wa kupita katika eneo hilo hasa kipindi cha masika kutokana na kivuko cha awali kusombwa na maji.
"kipindi cha masika akina mama walikuwa wanajifungulia hapa, wanafunzi kwenda shule mpaka wapatikane watu wa kuwavusha, wengine wanavushwa kwa pesa, Mwenyekiti wa Serikali ya mtaa na wajumbe wake walikuwa wanakaa hapa kusubiri kuwavusha watoto ilikuwa ni adha kubwa sana" .
Amesema kwa hatua iliyofikia ya ujenzi wa daraja hilo ni furaha kubwa sana kwao na kwamba kilio cha wakazi wa Butengwa kimeisha na kuongeza kuwa daraja hilo limeleta tabasamu kwa wakazi wa mtaa wa Botengwa na Kata ya Ndembezi kwa ujumla.
Naye Meneja wa Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) Mhandisi Samson Pamphili amesema kuwa wakati wa masika eneo hilo lilikuwa halipitiki kutokana na mafuriko makubwa ambayo yalisababishwa na mvua hivyo walilipa kipaumbele kwenye mipango yao kwa kujenga daraja kupitia chanzo chochote cha pesa.
Amesema wamebahatika kupata fedha za kutekeleza kazi hiyo kiasi cha shilingi 105,477,950 kupitia Mfuko wa Dharura (CERC) ambao unafadhiliwa na Benki ya Dunia na unalenga kuboresha miundombinu ya barabara iliyoharibiwa na mafuriko.
Ameongeza kuwa muda wa ujenzi wa daraja hilo ni miezi sita na kwamba ujenzi ulianza Desemba 29, 2025 na unatarajia kukamilika Juni 28, 2026 lakini kwa mujibu wa Mhandisi Pamphili ujenzi wa daraja hilo umefanyika kwa haraka na mpaka sasa umefikia asilimia 93 na ifikapo Machi 28, 2026 daraja hilo litaanza kutumika.
Kwa upande wake Emmanuel Exavery Hanya Mkazi wa mtaa wa Botengwa amesema eneo hilo lilikuwa ni tishio kabla ya ujenzi wa daraja hilo na kuongeza kuwa walikuwa wakipata shida kuvuka eneo hilo kipindi cha masika hasa wanafunzi kwenda shuleni, akina mama wajawazito na waliokuwa wakienda kwenye shughuli zao za kiuchumi.
"Tunaishukuru serikali kwa usikivu wao kwa kuja kutatua changamoto iliyokuwepo kwenye eneo hili na kufikia hatua hii, hivyo changamoto kwenye eneo hili zimeisha na wananchi tunaweza kuvuka bila shida yeyote".



.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)





.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)


.jpeg)


.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)


