Na Nasra Ismail, Geita

Mbunge wa Jimbo la Bukombe, Dkt. Doto Biteko, amemwagia sifa Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (MNEC) Mkoa wa Geita, Gervas Evarist, akimtaja kama mhimili muhimu katika kuimarisha chama mkoani humo kupitia uboreshaji wa miundombinu.

Akizungumza kwenye mikutano ya shukrani kufuatia ushindi wa CCM katika Uchaguzi Mkuu wa 2025, Dkt. Biteko alibainisha kuwa mchango wa kifedha wa MNEC Evarist umewezesha ujenzi wa ofisi za kisasa katika kata mbalimbali, hususan wilayani Bukombe. 

Alieleza kuwa hatua hiyo ni kielelezo cha uongozi unaojali hadhi ya chama.Katika ziara hiyo iliyopita kwenye kata za Bulega, Bugelenga, Iyogelo, na Ng’anzo, Dkt. Biteko aliambatana na Mwenyekiti wa CCM Wilaya, Matondo Lutondo, ambapo alijionea miradi mbalimbali ikiwemo majengo ya biashara na nyumba za kulala wageni zinazomilikiwa na chama.

"Viongozi wanapimwa kwa kazi na si maneno. Uwepo wa ofisi bora na miradi ya kiuchumi ni siri ya utulivu na mafanikio ya chama chetu katika ngazi ya kata," alisisitiza Dkt. Biteko.

Mbali na masuala ya chama, Dkt. Biteko aliahidi kutoa mabati kwa ajili ya Zahanati ya Mtinga, huku Mwenyekiti wa Halmashauri, Erick Kagoma, akiwahimiza wananchi kuchangamkia mikopo ya 10% ya halmashauri ili kujiletea maendeleo.







Kiongozi wa Mbio za mwenge wa Uhuru kitaifa mwaka 2026 Wazo Mwang'onda ameridhishwa na kasi ya ujenzi wa mradi wa barabara ya Bohari yenye urefu wa mita 600 inayojengwa kwa kiwango cha lami katika mtaa wa Bohari Kata ya Mwenge Manispaa ya Lindi wenye thamani ya zaidi ya milioni 466

Akizungumza mara baada ya kuweka jiwe la msingi Leo Mei 2, 2026 Mwang'onda amewapongeza Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini TARURA kwa usimamizi mzuri wa Mradi huo ambao utachochea shughuli za kiuchumi kwa wananchi wa eneo hilo.

Awali akisoma taarifa mbele ya kiongozi huyo wa mbio za mwenge wa Uhuru mwaka 2026 Meneja wa TARURA Wilaya ya Lindi Mhandisi Downson Paschal amesema Mradi huo unaotekelezwa kwa fedha za Mfuko wa Mafuta   utekelezaji wake umefikia asilimia 90.

Amesema mkandarasi anayetekeleza mradi huo ni kampuni ya SEC ya Mtwara, ambapo ujenzi ulianza Septemba 20, 2024 na unatarajiwa kukamilika Mei 28, 2026 ukiwa na lengo la kuboresha miundombinu ya usafiri na kuchochea shughuli za kiuchumi kwa wananchi wa eneo hilo.

Ameongeza  kuwa hadi sasa kazi mbalimbali zimekwisha fanyika ikiwemo kusafisha eneo la barabara, kujenga tabaka la msingi pamoja na uwekaji wa mifereji na makalavati ili kuhakikisha barabara hiyo inadumu kwa muda mrefu.

Aidha amebainisha  kuwa kukamilika kwa mradi huo kutasaidia kurahisisha usafiri na usafirishaji wa bidhaa, kupunguza changamoto ya vumbi pamoja na kuongeza kasi ya maendeleo ya kiuchumi kwa wakazi wa Kata ya Mwenge wa Uhuru na maeneo jirani.

Baadhi ya wananchi wa Manispaa hiyo ya Lindi wameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha za maendeleo ya miundombinu,  huku wakibainisha kuwa hatua hiyo imesaidia kuboresha huduma za kijamii na kiuchumi kwa wananchi.











Farida Mangube, Morogoro
CHUO Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimesisitiza kuwa mafanikio yake katika tafiti, ufundishaji na utoaji wa huduma kwa jamii yanategemea kwa kiasi kikubwa mchango wa wafanyakazi wake, huku kikiahidi kuendelea kuboresha mazingira ya kazi ili kuongeza tija na ustawi kazini.

Akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi), kwa niaba ya Makamu Mkuu wa Chuo, Prof. Raphael Chibunda, Naibu Makamu Mkuu wa Chuo upande wa Mipango, Fedha na Utawala, Prof. Amandus Muhairwa, amesema uongozi wa Chuo umejipanga kushughulikia changamoto mbalimbali zinazowakabili wafanyakazi na kuimarisha mazingira rafiki ya utendaji kazi.

Akijibu risala ya wafanyakazi, Prof. Muhairwa alieleza kuwa Menejimenti imepokea kwa uzito maoni, changamoto na mapendekezo yaliyowasilishwa, na itaendelea kuyafanyia kazi kupitia mifumo rasmi ya uongozi kwa lengo la kupata suluhisho endelevu.

Alibainisha kuwa SUA inaendelea kuboresha upatikanaji wa vitendea kazi kwa kuimarisha mifumo ya manunuzi na kushirikiana na wazabuni wenye uwezo wa kutoa huduma kwa wakati na kwa viwango vinavyokidhi mahitaji ya taasisi.

Aidha, alikiri kuwepo kwa changamoto ya uhaba wa ofisi, akieleza kuwa hali hiyo imetokana na ongezeko la watumishi ambapo jumla ya wafanyakazi 263 wameajiriwa katika kipindi cha miaka sita iliyopita, huku 125 wakistaafu, hali iliyoongeza shinikizo la miundombinu ya ofisi.

Prof. Muhairwa alisisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano, uwajibikaji na maadili kazini, akihimiza utamaduni wa kuheshimiana miongoni mwa wafanyakazi kwa kauli mbiu: “Mkubwa amheshimu mdogo na mdogo amheshimu mkubwa.”

Awali, Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa RAAWU tawi la SUA, Bw. Faraja Kamendu, pamoja na Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi THTU tawi la SUA, Dkt. Nickson Mkiramweni, waliwasilisha risala ya wafanyakazi wakieleza changamoto mbalimbali zinazowakabili, huku wakisisitiza umuhimu wa mshikamano, heshima na ushirikiano kazini.

Viongozi hao walieleza kuwa wana imani na utayari wa Menejimenti katika kushughulikia hoja zilizowasilishwa, na kuwahimiza wafanyakazi kujiunga na vyama vya wafanyakazi ili kulinda haki na maslahi yao kwa ufanisi zaidi.





KAMA ulikuwa unasubiri nafasi ya kuanza kutengeneza pesa kwa njia ya kisasa na ya uhakika, basi huu ndiyo wakati wako. Meridianbet wamekuja na bonge la ofa inayoitwa Drops & Wins, ambapo ushindi unakuja moja kwa moja bila kusubiri. Hapa mambo ni mubashara, unacheza sasa hivi na una nafasi ya kushinda papo hapo, bila stori ndefu.

Ili kuanza, unachotakiwa kufanya ni kujiunga na Meridianbet, kisha uingie kwenye kasino yao na uchague michezo ya Pragmatic Play unayoipenda. Ukishaweka dau lako na kuanza kucheza, tayari unakuwa kwenye nafasi ya kushinda. Kila raundi inakuweka karibu zaidi na ushindi mkubwa.

Vilevile, Michezo mingi zaidi ya kubashiri inaendelea kupatikana ndani ya Meridianbet ikiwa na ODDS kubwa na machaguo mengi zaidi. Kushiriki ni vyepesi kupitia tovuti ya MERIDIANBET au kwa kupiga *149*10#.

Uzuri wake ni kwamba unaweza kushinda hadi mara 100,000 ya dau lako. Pia kuna ofa ya mizunguko ya bure ambayo inakuja kama bonasi, ikikupa nafasi nyingine ya kushinda bila kutumia pesa yako tena. Hii inaongeza nafasi zako za kuondoka na mkwanja mzito.

Kitu kinachovutia zaidi kwenye Drops & Wins ni kwamba hakuna kusubiri. Matokeo ni ya papo hapo, unajua hapo hapo kama umechukua mzigo wako. Kila mchezo una nafasi yake ya kutoa ushindi mkubwa ndani ya muda mfupi, na ndiyo maana watu wengi tayari wanafaidika nayo.

Mtaa tayari umeamka na watu wanapiga pesa, usibaki nyuma ukiangalia tu. Jiunge na Meridianbet leo, anza kucheza na ujaribu bahati yako. Hii inaweza kuwa hatua yako ya kubadilisha mchezo kabisa na kuanza kushinda.

WANANCHI wanaozunguka Hifadhi ya Taifa Kitulo mkoani Njombe wameendelea kunufaika kiuchumi kupitia ongezeko la matukio ya utalii wa michezo, huku mbio za Kitulo Garden Marathon zikionekana kuwa kichocheo kipya cha ajira na biashara ndogo ndogo katika maeneo hayo.

Katika tukio hilo lililofanyika Mei 2, 2026, wakazi wa Wilaya ya Makete na maeneo ya jirani walijitokeza kwa wingi kuuza bidhaa na kutoa huduma mbalimbali kwa washiriki na wageni, hatua iliyosaidia kuongeza kipato cha kaya na kupunguza utegemezi wa shughuli hatarishi kama ujangili.

Akizungumza wakati wa mbio hizo, Mkurugenzi wa Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), Ephraim Mafuru, alisema kuwa utalii wa michezo umeendelea kuwa daraja muhimu la kuwaunganisha wananchi na fursa za kiuchumi zinazotokana na rasilimali za asili.

Alieleza kuwa kupitia huduma za malazi, chakula, usafiri na uuzaji wa bidhaa za mikono, wananchi wengi wameweza kujiongezea kipato na kuboresha maisha yao, huku akisisitiza kuwa sekta ya utalii ni jumuishi na inagusa watu wa kada mbalimbali.

Mbali na faida za kiuchumi, marathon hiyo pia imechangia maendeleo ya kijamii baada ya kompyuta 40 kutolewa kwa shule nane za sekondari wilayani Makete, hatua inayolenga kuinua kiwango cha elimu kwa vijana wa eneo hilo.

Kwa upande wa uhifadhi, viongozi wa TANAPA wamesema matukio kama hayo yanaongeza uelewa wa wananchi juu ya umuhimu wa kulinda hifadhi, kwani yanawaonesha moja kwa moja manufaa ya kiuchumi yanayotokana na rasilimali hizo.

Kitulo Garden Marathon, iliyojumuisha mbio za kilomita 5, 10 na 21, imeendelea kujijengea umaarufu kama jukwaa la kukuza afya, kutangaza vivutio vya utalii na kuimarisha uchumi wa jamii zinazozunguka hifadhi hiyo.








Wananchi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma wametakiwa kutumia kikamilifu fursa ya Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia ili kupata huduma muhimu za kisheria na vyeti kwa wakati, badala ya kusubiri hadi wanapokumbana na changamoto zinazohitaji nyaraka hizo. 

Wito huo umetolewa huku kukisisitizwa kuwa uwepo wa wataalamu wa Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA) katika kampeni hiyo ni nafasi adhimu ya kupata ushauri na msaada  wa moja kwa moja kuhusu masuala ya Wosia, Ndoa, Talaka, vyeti na mirathi.

Akizungumza Mei 2, 2026, Afisa Msajili Mwandamizi kutoka RITA Dodoma, Mwinyijuma Maneno Moshi, ametoa rai hiyo na  kuwahimiza wananchi kujitokeza kwa wingi kutembelea banda la taasisi hiyo katika maadhimisho ya utoaji wa huduma za msaada wa kisheria yanayoendelea mkoani Dodoma.

Kampeni hiyo, inayoratibiwa na Wizara ya Katiba na Sheria, inaendelea kwa muda wa siku 15 kuanzia Mei 1, 2026, na inafanyika katika viwanja vya Mtekelezo vilivyopo jijini Dodoma.

Moshi amesema kuwa ndani ya kipindi hicho, RITA inatoa huduma mbalimbali ikiwemo usajili mpya wa vyeti vya kuzaliwa, kubadilisha vyeti vya zamani, pamoja na uhakiki wa vyeti vya kuzaliwa ambapo mwananchi ataweza kupata cheti chake ndani ya masaa machache.

Aidha, huduma nyingine zinazotolewa ni pamoja na utoaji wa vyeti vya vifo, vyeti vya ndoa pamoja na talaka, lengo likiwa ni kurahisisha upatikanaji wa nyaraka muhimu kwa wananchi.

Mbali na hilo, Moshi amewahimiza Watanzania kutembelea banda la RITA ili kupata elimu kuhusu umuhimu wa kuandika wosia, ameeleza kuwa wosia husaidia katika mgawanyo wa mali pindi mtu anapofariki, ambapo mmoja wa mashahidi atatakiwa kutoa taarifa RITA na kufuatiwa na taratibu za kuwasilisha wosia katika sehemu husika.

Ametaja faida za kuandika na kuhifadhi wosia RITA kuwa ni pamoja na taasisi hiyo kuwa ya serikali isiyo na ukomo wa maisha, kuwa na wataalamu wa sheria waliobobea katika masuala ya mirathi, uwepo wa sehemu salama ya kuhifadhi wosia pamoja na gharama nafuu za huduma hiyo.




▪️︎ Asema ujenzi uendelee hadi kukamilisha km 58 zote kwa kiwango cha lami

▪️︎ Asisitiza kukamilishwa kwa usanifu na upatikanaji wa fedha kwa wakati

Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, ameridhishwa na utekelezaji wa ujenzi wa barabara ya Mtili–Ifwagi–Mdabulo–Lulanda (km 58) kwa kiwango cha lami, huku akiagiza hatua za haraka zichukuliwe kukamilisha sehemu zilizosalia ili barabara hiyo iweze kutoa huduma kwa ukamilifu.

Amesema hayo leo Jumamosi, Mei 2, 2026, alipotembelea na kukagua mradi huo katika Wilaya ya Mufindi, mkoani Iringa, ambapo alipokea taarifa ya utekelezaji na kujionea maendeleo ya ujenzi uliofikia hatua mbalimbali.

“Nimeambiwa tayari kilomita kumi na nne zimeshajengwa na nimeona… tutaendelea kujenga barabara hii kwa sababu bado kuna kilomita zingine, ili iweze kutoa huduma kwa ukamilifu wake,” amesema.

Mradi huo unatekelezwa kupitia mpango wa Roads to Inclusion and Socio-Economic Opportunities (RISE) unaofadhiliwa kwa ushirikiano kati ya Serikali na Benki ya Dunia, ukiwa na lengo la kuboresha miundombinu ya barabara vijijini, kukuza uchumi na kuongeza fursa za ajira kwa wananchi.

Kwa mujibu wa taarifa ya mradi, hadi sasa ujenzi wa kipande cha Mtili–Ifwagi (km 14) umekamilika kwa asilimia 100 kwa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni 21, huku mradi mzima ukiwa umefikia takriban asilimia 57 ya utekelezaji katika awamu mbalimbali.

Akizungumzia hatua zinazofuata, Waziri Mkuu amesisitiza umuhimu wa kuharakisha usanifu wa sehemu zilizosalia ili kuuwezesha mradi kuingizwa kwenye bajeti na kuanza ujenzi wake kwa wakati.

“Ikamilisheni haraka usanifu… mpaka tunapomaliza mwezi wa sita tujue mmefikia hatua gani ili tuweze kusukuma masuala ya fedha na utekelezaji wake uanze mara moja,” amesema.

Aidha, ameeleza kuwa barabara hiyo ni ya kimkakati kwa uchumi wa eneo hilo kutokana na mchango wake katika usafirishaji wa mazao ya misitu, chai na mazao mengine ya kilimo.

“Barabara hii ni barabara muhimu, ni barabara ya kiuchumi… magari yanabeba mbao na mazao ya viwandani, wakati mwingine yanakwama, sasa ni wakati wa kuijenga barabara hiyo,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amewataka wataalamu na wasimamizi wa mradi huo kufanya kazi kwa kasi na ubunifu ili kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati, akisisitiza kuwa hakuna sababu ya kuchelewesha miradi ya maendeleo yenye tija kwa wananchi.

“Ni barabara za uzalishaji… ikimbizeni hata kama mtafanya kazi usiku na mchana,” amesema.

Waziri Mkuu pia amewapongeza TARURA na wadau wa mradi kwa utekelezaji mzuri wa kipande kilichokamilika, hususan kwa kuzingatia usalama wa watumiaji wa barabara wakiwemo watembea kwa miguu.

Awali, taarifa ya mradi ilieleza kuwa kukamilika kwa kipande hicho cha barabara kumeongeza ufanisi wa usafiri na usafirishaji, kurahisisha upatikanaji wa huduma za kijamii, pamoja na kuchochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi katika Wilaya ya Mufindi na maeneo jirani.

Amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kuwekeza katika miundombinu ya barabara ili kuchochea maendeleo ya uchumi na kuboresha maisha ya wananchi.







Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ameyakaribisha makampuni na wawekezaji kutoka Uturuki kuwekeza nchini, hususan katika sekta za biashara, nishati na miundombinu.

Rais Dkt. Mwinyi ametoa wito huo leo, tarehe 02 Mei 2026, alipokutana na Mkurugenzi Mkuu anayeshughulikia masuala ya Afrika kutoka Wizara ya Mambo ya Nje ya Uturuki, Balozi Volkan Isikci, aliyefika Ikulu, Zanzibar, akiongozana na Balozi wa Uturuki nchini Tanzania, Balozi Bekir Geze.

Amesema hatua hiyo itasaidia kui
marisha uhusiano wa kihistoria kati ya nchi hizo mbili na kufungua fursa mpya za ushirikiano katika biashara na uwekezaji

Aidha, a.mesisitiza umuhimu wa wawekezaji kuwekeza katika sekta za kimkakati zikiwemo nishati, kilimo, utalii, afya na miundombinu, pamoja na kuongeza thamani ya mazao ya ndani.

Kwa upande wake, Balozi Isikci ameihakikishia Zanzibar kuendelea kushirikiana na kuunga mkono juhudi za maendeleo ya kiuchumi kupitia sekta mbalimbali ikiwemo elimu, afya, kilimo na utalii.













▪️︎ Aagiza TANROADS kumpata mkandarasi ndani ya wiki mbili

▪️︎ Aelekeza fedha za awali zitolewe mara moja kuanza ujenzi

Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, ameagiza kuanza mara moja ujenzi wa barabara za Nyololo–Mtwango (km 40) na Mafinga–Mgololo katika Jimbo la Mufindi Kusini, mkoani Iringa, akisisitiza kuwa ahadi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ni maelekezo ya moja kwa moja yanayopaswa kutekelezwa bila kuchelewa.

Ameyasema hayo leo Jumamosi, Mei 2, 2026, alipofanya ziara ya kikazi katika Jimbo hilo na kuzungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi Igowole, kata ya Igowole, ambapo pia alisikiliza kero na mahitaji mbalimbali ya wananchi.

Akizungumza katika mkutano huo, Dkt. Nchemba amesema Serikali inaendelea kutekeleza Ilani ya Chama Cha Mapinduzi kwa vitendo na kuleta matokeo kwa wananchi.

“Mheshimiwa Rais amejitambulisha kwa kazi zake kwamba yeye ni mtu wa matokeo,” amesema.

Katika hatua ya kuharakisha utekelezaji wa miradi ya miundombinu, Waziri Mkuu ameagiza kuanza mara moja kwa ujenzi wa barabara hizo na kusisitiza kuwa hakuna sababu ya kuchelewesha utekelezaji wa ahadi za Rais.

Akijibu hoja kuhusu barabara ya Nyololo–Mtwango, ameielekeza TANROADS Mkoa wa Iringa kuhakikisha mkandarasi anapatikana ndani ya wiki mbili ili kazi ianze mara moja.

“Sitaki majibizano ya barua ya vibali kwenye jambo ambalo Rais ameelekeza… tafuteni mkandarasi, ndani ya wiki mbili mniambie mmempata mkandarasi,” amesema.

Aidha, amemtaka Mkuu wa Mkoa wa Iringa kusimamia kwa karibu utekelezaji wa agizo hilo, akisisitiza kuwa ahadi ya Rais ni ya kutekelezwa kwa ukamilifu wake.

“Ahadi ya Rais mnajengaje mita 200, 200?” amesema.

Kuhusu barabara ya Mafinga–Mgololo, Waziri Mkuu amemuagiza Katibu Tawala wa Mkoa kuandika barua mara moja kwenda Wizara ya Fedha kwa ajili ya kupatiwa fedha za malipo ya awali ili mradi huo uanze bila kuchelewa.

“Andikeni barua leo leo, pelekeni Wizara ya Fedha kupewa advance payment… na nakala nileteeni ofisini kwangu Jumatatu niione. Mradi huu uanze mara moja,” amesema.

Katika mkutano huo, Waziri Mkuu pia alisikiliza kero mbalimbali za wananchi, ikiwemo madai ya malipo dhidi ya kampuni ya Leshenia Investment inayodaiwa kutowalipa baadhi ya wananchi waliotoa huduma au kufanya biashara nayo.

Akizungumzia suala hilo, amesema Serikali haitavumilia vitendo vya kunyanyasa wananchi na kuchelewesha haki zao.

“Nachukia sana unyang’anyi wa haki za watu… malipo ya hawa vijana wanaodai huko viwandani na kwenye kampuni hiyo yalipwe mara moja. Mkuu wa Mkoa simamia hili mara moja,” amesema.

Ameongeza kuwa hatua kali zitachukuliwa dhidi ya wadaiwa watakaokaidi maagizo hayo.

“Mkuu wa Mkoa na RPC watafuteni, wajisalimishe, wasipojisalimisha wakamateni… ninaporudi nataka nikute wamelipa,” amesema.

Amesisitiza kuwa Serikali ipo kulinda haki za wananchi na haitaruhusu mtu yeyote kunyimwa malipo yake halali.

Awali, Waziri Mkuu alipita katika Kijiji cha Idofi, Mji wa Makambako, mkoani Njombe, ambapo aliwasalimia wananchi na kupokea taarifa kuhusu mradi wa umwagiliaji pamoja na soko la mbogamboga, sambamba na kusikiliza changamoto za wananchi wa eneo hilo.

Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kusini ambaye pia ni Naibu Waziri wa Uchukuzi, Mheshimiwa David Mwakiposa Kihenzile, amesema changamoto ya barabara imekuwa kikwazo kikubwa kwa shughuli za kiuchumi, hususan kwa wakulima kusafirisha mazao yao na viwanda kupata malighafi kwa wakati.











Top News