Picha na Amour Nassor,
Habari na Penzi Nyamungumi – Magu
Makamu wa Rais Dk. Mohammed Gharib Bilal amewataka viongozi nchini kuhamasisha wananchi kuhusu matumizi ya teknolojia ya uvunaji wa maji ya mvua ili kupunguza tatizo la maji linalojitokeza katika maeneo mbalimbali ya nchi.
Akizungumza baada ya kufungua shule ya sekondari Kitumba iliyoko katika wilaya ya Magu mkoani Mwanza Dk. Bilal alisema teknolojia ya uvunaji wa maji ya mvua itawawezesha wananchi kupata maji ya uhakika ambayo yatahifadhiwa kwa matumizi ya baadaye badala ya kuyaacha maji hayo kuishia ardhini.
Dk. Bilal ambaye alitoa shilingi milioni tatu ili zitumike kujenga miundo mbinu ya kuvuna maji ya mvua katika shule hiyo alisema utaratibu huo usiishie shuleni hapo bali wananchi wahamasishwe umuhimu wa kuvuna maji ya mvua kwa manufaa yao.
“Tusiishie hapa, utaratibu huo uenee katika sehemu nyingine. Wananchi wahamasishwe wanapojenga nyumba zao ni muhimu wakumbuke kujenga mbiundombinu ya kuvuna maji ya mvua,” alidokeza Makamu wa Rais na kuongeza
“Tuchukue changamoto hii, tuhakikishe tunavuna maji ya mvua…hii itatusaidia kupunguza tatizo la maji nchini.”
Awali, akitoa taarifa Mkuu wa wilaya ya Magu Bibi Zainab Kondo alimweleza Makamu wa Rais kuwa wilaya imekuwa ikitilia mkazo teknolojia ya uvunaji wa maji ya mvua na mpaka sasa matanki 26 ya kuvuna maji ya mvua kwenye mapaa ya nyumba yamejengwa.
Akizungumzia hali ya upatikanaji wa majisafi na salama alisema vijijini imeongezeka kutoka asilimia 53.7 mwaka 2000 hadi asilimia 62.6 mwaka 2010 na kwa upande wa Magu mjini ni asilimia 17 tu.
Alisema hali ya upatikanaji wa maji mjini Magu siyo nzuri kutokana na mradi kuchakaa, ulisanifiwa na kujengwa ili kuhudumia watu 6,000 tu mwaka 1974 na sasa unahudumia zaidi ya watu 37,000.
“Zabuni ya kumpata mkandarasi wa kujenga mradi huu wa Magu Mjini inategemewa kufanyika mwezi Mei, mwaka huu, kwa mujibu wa Mpango kazi wa Mtaaalmu Mshauri aliyepewa kuandaa michoro, kuusanifu na kukadiria gharama,” alibainisha Mkuu huyo wa wilaya.
Hata hivyo Bibi Kondo alisema wilaya imekuwa ikichukua hatua mbalimbali katika kuboresha huduma ya utoaji majisafi na salama ikiwa ni pamoja na kuchimba visima virefu 51 na vifupi 3 katika kipindi cha mwaka 2005 hadi 2010 na kukarabati visima 15 pamoja na miradi mitano ya maji ya bomba.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...