Kamisheni ya Umoja wa Mataifa ya Kugharamia Fursa za Elimu Duniani iliyo chini ya uenyekiti wa Waziri Mkuu Mstaafu wa Uingereza Mheshimiwa Gordon Brown imekamilisha kazi yake ya kuandaa Taarifa yenye mapendekezo ya kuiwezesha dunia kuhakikisha kila mtoto popote alipo duniani anapata fursa ya elimu ya ubora wa elimu unaolingana ifikapo mwaka 2030.
Kamisheni hiyo ya Elimu iliyoundwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa imefanya kikao chake cha majumuisho tarehe 2 Julai, 2016 jijini Oslo. Kufuatia Kikao hicho cha majumuisho kilichopitia ripoti ya Kamisheni na mapendekezo yake, ripoti ya Kamisheni sasa inatarajiwa kuwasilishwa kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa jijini New York tarehe 18 Septemba, 2016.
Akizungumza mara baada ya Kikao cha Kamisheni hiyo, Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete na mmoja wa Makamisha wa Kamisheni hiyo ameelezea matumaini yake kuwa mapendekezo yaliyomo kwenye ripoti iwapo yatatekelezwa yataiwezesha dunia kuhakikisha kuwa hakuna mtoto atakayeachwa nyuma kwa upande wa elimu bora ifikapo mwaka 2030 na kuendelea kama ilivyoazimiwa katika Malengo ya Dunia ya Maendeleo Endelevu (SDG).
Ameendelea kueleza kuwa ili kufikia lengo hilo, hapana budi viongozi wa dunia wafanye maamuzi ya kimapinduzi ili kuwezesha kupatikana kwa fedha zitakazowezesha kila mtoto kila mahali alipo duniani apate fursa ya elimu na elimu yenye ubora unaolingana.
Kamisheni hiyo inayoongozwa na Waziri Mkuu Mstaafu wa Uingereza
na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa wa Masuala ya Elimu inaundwa na jopo la watu mashuhuri wakiwemo Mawaziri Wakuu Wastaafu, Mawaziri Wastaafu, Wafanyabiashara na Matajiri Wakubwa kutoka Sekta Binafsi na Wanaharakati kutoka Asasi za Kiraia duniani.



Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...