Na Frank Shija –
MAELEZO.
Tanzania yadhamiria
kuimarisha uhusiano baina yake na Jamhuri ya Korea kwa kufungua Ofisi zake za
Ubalozi Mjini Seoul, nchini Korea.
Hayo yamebainishwa na
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Dkt. Augustine
Mahiga leo jijini Dar es Salaam wakati akipokea msaada wa Dola za Kimarekani
50,000 kwa ajili ya kusaidia urejeshaji wa miundombinu iliyoharibika kutokana
na Tetemeko la Ardhi lilitokea Mkoani Kagera mnamo tarehe 9 Septemba 2016.
Balozi Mahiga amesema
kuwa nchi ya Jamhuri ya Korea imekuwa na uhusiano mzuri na wa muda mrefu na
Tanzania ambapo kupitia uhusiano huo imekuwa ikisaidia katika mambo mbalimbali
ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya afya akitolea mfano Hospitali za
Mloganzila na Chanika ambazo zote zimejengwa kwa ufadhili wa Shirika la Kimataifa
la Mahusiano la Korea (KOICA).
“Korea imekuwa na Ofisi
za Ubalozi hapa nchini kwa zaidi ya miaka 25 hivyo wameona ni wakati sasa kwa
Tanzania kuwa na Ofisi yake Ubalozi nchini nnchini Korea,” Alisema Balozi
Mahiga.
Kwa upande wake Balozi
wa Jamhuri ya Korea nchini Bw. Song, Geum – Young amesema kuwa msaada huo
unatokana na namna ambavyo waliguswa na janga la Tetemeko la ardhi lililotokea
Mkoani Kagera na kusababisha uharibifu mkubwa wa miundombinu na makazi ya
wananchi.
Ameongeza kuwa msaada
huo ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi aliyoitoa kwa Rais Dkt. Magufuli
alipomtembelea Ikulu na kumpa Pole mnamo tarehe 22 Septemba mwaka huu.
Balozi Song Geum-Young
pia amemhakikishia Waziri Mahiga kuwa Korea itaendeleza na kuimarisha uhusiano
wake na Tanzania na kwamba itatoa ushirikiano wa kutosha kufanikisha miradi ya
maendeleo ambayo inatekelezwa hapa nchini ikiwemo ujenzi wa Daraja la Salender,
Meli, Hospitali ya Mloganzila, Chanika na mingineyo.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...