SERIKALI ya Mkoa Mara kwa kupitia Katibu Tawala wake, Mheshimiwa Ado Mapunda, imewaagiza watendaji wa serikali mkoani humo kuhakikisha kompyuta walizopewa na Taasisi ya Kifedha ya Bayport Financial Services, zinaelekezwa kwenye shule za kata ili kuchangia ukuzaji wa kiwango cha elimu.

Mheshimiwa Mapunda aliyasema hayo mwishoni mwa wiki wakati anapokea kompyuta sita kutoka Bayport zilizoelekezwa katika Halmashauri ya Tarime, Rorya na Manispaa ya Musoma, huku kila ofisi ikipata kompyuta mbili ikiwa ni mwendelezo wa ugawaji wa vitendea kazi kutoka kwenye taasisi hiyo inayojihusisha na mikopo ya fedha taslimu kwa watumishi wa umma na wafanyakazi wa kampuni zilizoidhinishwa.

Akizungumza katika makabidhiano hayo, Katibu Tawala huyo alisema lengo la Mkoa wao ni kuona kiwango cha elimu kinapiga hatua kubwa, hivyo wameona msaada huo uelekezwe zaidi katika shule za kata kwa ajili ya kuhifadhi kumbukumbu muhimu za wanafunzi wao.Alisema kufanya hivyo kutaongeza ukuzaji wa elimu ya wanafunzi wa mkoani Mara, ili iwe njia ya kuandaa wataalamu wazuri kwa kutumia vema teknolojia ya kompyuta inayoboresha utendaji wa kazi.

“Tunashukuru wenzetu wa Bayport wa Kanda ya Ziwa pamoja na Makao Makuu kwa kutuletea msaada huu mkubwa kwetu ambao kwa hakika tutautumia vizuri katika Mkoa huu wa Mara ili ulete tija kama mlivyokusudia wakati mnafikiria kusambaza.

“Ofisi yetu imeagiza kompyuta hizi zisambazwe katika baadhi ya shule za kata kwa kuzitumia kwa namna moja ama nyingine ili wanafunzi wetu wasonge mbele zaidi kwa kuanzia kurekodi vizuri takwimu zao kama njia ya kugundua tunafanya juhudi za kutuvusha hatua ya juu zaidi,” Alisema Mapunda.

Naye Mratibu wa Masoko na Mawasiliano wa Bayport Financial Services, Mercy Mgongolwa, alisema ndoto zao zinaelekea kukamilika kuhakikisha kwamba msaada wa kompyuta zao unafika kwa haraka kama walivyokusudia na kuuzindua mwaka jana jijini Dar es Salaam.

“Kompyuta tulizotoa Mara na Kanda ya Ziwa ni mwendelezo wetu wa kutoka kwenye kompyuta 125 tulizomkabidhi Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, huku 80 zikielekezwa mikoani na kuufanya mzigo wote ufikie 205 wenye thamani ya Sh Milioni 500,” Alisema Mercy.

Mbali na Mara, Bayport pia walikabidhi kompyuta mbili kwa Halmashauri ya Wilaya Misungwi, mkoani Mwanza na kuifanya Kanda ya Ziwa kuvuna kompyuta nane za taasisi hiyo ambapo pia ilitangaza kuwa utaratibu huo wa kufikisha kompyuta utaendelea katika wilaya na mikoa mbalimbali ya Tanzania Bara wakiamini utasaidia kuongeza ufanisi katika ofisi za umma.
Mratibu wa Masoko na Mawasiliano wa Bayport Financial Services, Mercy Mgongolwa, akimkabidhi kompyuta sita Katibu Tawala wa Mkoa wa Mara, Mheshimiwa Ado Mapunda kwa ajili ya kuongeza ufanisi katika ofisi za umma mkoani Mara. Wengine kwenye tukio hilo ni watumishi wa Bayport, akiwamo Meneja wa Kanda ya Ziwa wa Bayport, Lugano Kasambala wa kwanza kushoto. Picha na Mpiga Picha Wetu Mara.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...