Imeelezwa kuwa jumla ya wanawake 47 wamehitimu mafunzo ya ukataji na ung’arishaji wa madini ya vito yanayotolewa na Kituo cha Jemolojia jijini Arusha ambacho kipo chini ya Wizara ya Nishati na Madini.

Hayo yalisemwa jijini Arusha na Kaimu Mratibu wa Kituo hicho, Erick Mpesa wakati wa Mnada wa Pili wa Kimataifa wa Madini ya Tanzanite unaofanyika jijini Arusha katika Kituo hicho.

Mpesa alisema kuwa mafunzo hayo yalianza kutolewa mwaka 2014 ambapo katika Awamu ya kwanza wanafunzi 15 walihitimu, Awamu ya Pili walihitimu wanafunzi 14 na Awamu ya Tatu walihitimu wanafunzi 18.
Mkufunzi Msaidizi katika Kituo cha Jemolojia Arusha, (TGC), Lilian Petro (wa kwanza kulia) akionyesha madini ya vito yaliyong’arishwa na wanafunzi wanaopata mafunzo katika Kituo hicho kilicho chini ya Wizara ya Nishati na Madini. Wa Pili kulia ni Mkurugenzi wa Kitengo cha Uthamini wa Madini ya Almasi na Vito (TANSORT), Archard Kalugendo, wa Pili kushoto ni Mhe. Catherine Magige, Mbunge wa Viti Maalum (CCM) na wa kwanza kushoto ni Beatrice Lupi, Mhasibu Mkuu kutoka Shirika la Madini la Taifa (STAMICO).

“Mafunzo haya hutolewa kwa muda wa miezi Saba ambapo Wanafunzi hawa ambao huwa na umri wa chini ya miaka 30 wanafadhiliwa na Mfuko wa Kuwaendeleza Wanawake chini ya Kamati ya Maonesho ya Vito ya Arusha (AGF) na Wizara ya Nishati na Madini,” alisema Mpesa.

Mratibu wa TGC aliongeza kuwa Kituo hicho pia kinaendesha shughuli za uchongaji wa mawe ya miamba kwa kutengeneza vinyago vyenye maumbo mbalimbali kama ya wanyama, ndege, samaki na vitu mbalimbali vya urembo.

Akizungumzia mafanikio ya kituo hicho, Mpesa alisema kuwa mbali ya kusaidia wanawake hao kupata mafunzo yatakayowasaida kujiajiri au kuajiriwa, Kituo hicho ni cha pekee Afrika Mashariki kinachoendeleza taaluma ya uongezaji thamani madini ya vito na miamba.
Mmoja wa wanafunzi katika Kituo cha Jemolojia Arusha, Zuwena Mtoo, akionesha utaalam wa kukata na kung’arisha madini ya Vito, baada ya kupata mafunzo katika Kituo hicho kilicho chini ya Wizara ya Nishati na Madini.

Kuhusu mipango ya kuendeleza Chuo hicho alisema kuwa, Chuo kimepanga kutoa mafunzo ya muda mrefu kwa ngazi ya diploma ambapo mitaala ya kozi mbalimbali za taaluma ya vito na usonara imeandaliwa na kuwasilishwa katika Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) ambapo mchakato wa ithibati na usajili unaendelea.

Kwa upande wake Mkufunzi Msaidizi wa TGC, Lilian Petro, alisema kuwa mafunzo hayo husaidia wanafunzi hao kutambua madini ya aina mbalimbali, kuyakata na kufahamu thamani ya madini husika.

Aidha Lilian, Alitoa ushauri kwa wanawake mbalimbali nchini kujiunga katika fani hiyo ya ukataji na ung’arishaji wa madini ya vito kwa kuwa inamsaidia mtu kujiajiri kwa kuanzisha vituo vya ung’arishaji wa madini ya vito ndani ya nchi na pia kuajiriwa.
Samadu Mohamed, kutoka Kituo cha Jemolojia Arusha, akionesha moja ya vinyago vinavyotokana na mawe ya miamba vinavyotengenezwa katika kituo hicho.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...