Shirika la Reli Tanzania (TRL) limepata hasara ya takribani shilingi bilioni tano katika kipindi cha mwezi mmoja baada ya njia ya reli ya kati kusombwa na mafuriko katika Wilaya ya Kilosa mkoani Morogoro na Gulwe mkoani Dodoma.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa wakati wa ziara ya kukagua maendeleo ya ukarabati wa miundombinu ya reli hiyo na kusema kuwa Serikali imejipanga kupata suluhisho la kudumu la uharibifu katika maeneo hayo ambapo mara kadhaa yamekuwa yakiathiriwa na mvua kutokana na mabwawa yaliyopo kujaa mchanga na hivyo kusababisha uharibifu huo.
“Serikali kwa sasa inayafanyia kazi mapendekezo matatu yaliyowasilishwa na RAHCO ikiwemo kuihamisha reli kwenye milima jirani, kuihamishia eneo ambapo inajengwa reli ya kisasa ya SGR ama kujenga tuta kubwa, huku tukizingatia gharama halisi za kazi hiyo kabla ya kufanya maamuzi”, amesema Prof. Mbarawa.
Mhandisi Mkuu kutoka Shirika la Reli (TRL), Mhandisi Nelson Ntejo akitoa maelezo kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (kulia) kuhusu maendeleo ya kazi ya ukarabati wa eneo lililoathiriwa na mvua kubwa zilizonyesha mwanzoni mwa mwaka, katika eneo la Kilosa mkoani Morogoro, wakati Waziri huyo alipokagua reli hiyo Mkoani humo, hivi karibuni.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa, akitoa maelekezo kwa Mhandisi Mkuu kutoka Shirika la Reli (TRL), Mhandisi Nelson Ntejo, alipokagua ukarabati wa njia ya reli ya kati ya eneo la Kilosa mkoani Morogoro iliyoharibiwa na mvua kubwa zilizonyesha mwanzoni mwa mwaka huu. Kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Dkt. Stephen Kebwe.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa, akikagua kazi zinazoendelea katika eneo la Kilosa, ambapo ukarabati umekamilika na treni za mizigo zimeanza kupita.
Muonekano wa sehemu ya njia ya reli ya kati eneo la Kilosa iliyokarabatiwa baada ya kuharibiwa na mvua kubwa zilizonyesha, mkoani Morogoro mwanzoni mwa mwaka huu.
Muonekano wa treni ya mizigo ikianza safari zake katika stesheni ya Kilosa, mkoani Morogoro kuelekea mkoani Mwanza mara baada ya njia hiyo kukarabatiwa.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...