Na: Veronica Kazimoto
Maafisa Habari, Mawasiliano na Uhusiano Serikalini wameombwa kuwa mabalozi wazuri katika sehemu zao za kazi na katika jamii wanayoishi kwa kuwaelimisha wananchi masuala mbalimbali yanayohusu kodi.
Akizungumza wakati akiwasilisha mada kuhusu Umuhimu wa Kodi kwenye Kikao Kazi cha Maafisa hao kinachoendelea jijini Arusha , Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipakodi kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Richard Kayombo, alisema elimu ya kodi itawafikia watu wengi zaidi kwa kuwa maafisa hao wana ushirikiano mkubwa katika kutoa habari sahihi kwa umma.
"Kila mmoja wetu anachokifanya ni sauti kwa mwenzake mahali alipo, ndio maana hata katika mitandao mbalimbali tumekuwa tukisaidiana kwa kuwa, ukiona jambo baya linasemwa juu ya taasisi ya mwenzako au Serikali unamsaidia kutoa ufafanuzi, hivyo, mkielewa mada yangu hapa, najua mtanisaidia kuelimisha masuala ya kodi katika sehemu zenu za kazi na maeneo mengine", alisema Kayombo.
Kayombo alisema kuwa, maafisa hao wana nafasi kubwa katika kuelimisha jamii na kusahihisha baadhi ya wananchi ambao wanakuwa na elimu isiyo sahihi kuhusu masuala yanayohusu kodi na ukusanyaji wa mapato kwa ujumla.
Aidha, pamoja na mambo mengine, Richard Kayombo aliwakumbusha Maafisa hao suala zima la kudai risiti kila wakati wanaponunua bidhaa ili kuchangia maendeleo ya nchi.
Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipakodi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Bw. Richard Kayombo, akiwasilisha mada kuhusu Umuhimu wa Kodi kwenye Kikao Kazi cha Maafisa Habari, Mawasiliano na Uhusiano Serikalini kinachoendelea jijini Arusha. Kikao hicho kinatarajia kumalizika tarehe 16 Machi, mwaka huu. (Picha na Benedict Liwenga).
KUSOMA ZAIDI BOFYA HAPA
KUSOMA ZAIDI BOFYA HAPA



Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...