WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali itaendelea kuimarisha vyama vya msingi vya ushirika vya mazao ya kilimo na masoko vinavyozalisha mazao ya kimkakati ya biashara ya pamba, kahawa, korosho, chai na tumbaku.
Amesema katika mwaka 2018/2019, Serikali inalenga kuimarisha masoko ya mazao hayo kwa kuhamasisha mfumo wa stakabadhi ghalani ambapo mazao hayo yatazalishwa na kuuzwa kupitia vyama vya ushirika kwa njia ya minada.
Ametoa kauli hiyo leo (Jumatano, Aprili 4, 2018) Bungeni mjini Dodoma, wakati akiwasilisha taarifa ya mapitio ya utekelezaji wa kazi za Serikali kwa mwaka 2017/2018 na mwelekeo wa kazi za Serikali kwa mwaka 2018/2019 kwenye mkutano wa 11 wa Bunge.
Waziri Mkuu amesema pamoja na hatua hizo, Soko la Bidhaa ambalo limeshaanzishwa, litasaidia sana kuimarisha masoko ya mazao kwani yatakuwa yanauzwa kwa njia ya ushindani mkubwa huku wakulima wanaozalisha kwa ubora wakinufaika na bei ya juu zaidi.
“Serikali imeamua kuweka mkazo maalum wa kuyaendeleza kwa kasi mazao matano ya biashara ambayo ni chai, kahawa, korosho, pamba na tumbaku. Lengo ni kuongeza mapato ya wakulima, kuwa chanzo cha kuaminika cha malighafi katika uchumi wa viwanda, na kuendelea kuwa chanzo kikuu cha ajira na fedha za kigeni.
Amesema uamuzi wa kuongeza usimamizi katika uzalishaji wa mazao hayo makuu ya biashara unatokana na ukweli kwamba, kwa kipindi kirefu uzalishaji ulishuka kutokana na changamoto kadhaa.
“Miongoni mwa changamoto hizo ni kupungua tija katika uzalishaji, baadhi ya wakulima kuacha kulima mazao hayo kutokana na kukata tamaa kwa sababu mbalimbali zikiwemo vyama vya ushirika kutotekeleza vema wajibu wao, wizi, dhuluma na pia ushiriki mdogo wa maafisa kilimo katika kusimamia kilimo cha kitaalamu,” alisema.



Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...