Na. Atley Kuni na
Mathew Kwembe, OR TAMISEMI
Waziri wa Nchi
Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo
amewaagiza Wakuu wa Mikoa kusimamia zoezi la kuwatambua wazee wote nchini
katika mikoa yao na wahakikishe kuwa ifikapo tarehe 30 Juni, 2018 Mikoa yao
inawasilisha Ofisi ya Rais TAMISEMI orodha ya wazee katika mikoa yao.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jijini Dodoma leo, Mhe. Jafo
alisema kuwa tayari amekwishatoa maagizo kwa Katibu Mkuu Ofisi ya Rais TAMISEMI
kuhakikisha kuwa zoezi hilo linashirikisha ngazi zote za Mamlaka ya Serikali za
Mitaa.
Alisema ifikapo tarehe 15 juni 2018 anatarajia kuona kuwa zoezi hilo liwe
limekamilika katika ngazi ya kata ambapo Mtendaji wa Kata atapaswa
kuliwasilisha katika ngazi ya halmashauri kabla ya kufika ngazi ya Mkoa.
Pia alisema kuwa ifikapo tarehe 20 Juni, 2018 anatarajia kuwa zoezi hilo liwe
limekamilika katika ngazi ya halmashauri ambapo Mkurugenzi wa Halmashauri atapaswa
kuwasilisha taarifa ya utekelezaji katika ngazi ya mkoa tarehe 26 juni, 2018.
Waziri Jafo alieleza kuwa ifikapo tarehe 30 Juni, 2018 anatarajia kuwa ofisi ya
Katibu Tawala wa Mkoa iwasilishe taarifa hiyo katika Ofisi ya Rais TAMISEMI.
Akifafanua zaidi kuhusu umuhimu wa zoezi hilo Mhe.Jafo alisema kuwa serikali
imeamua kuchukua hatua hiyo ya kuwatambua wazee wote nchini ili wasiendelee
kupata manyanyaso kwa kukosa utambuzi rasmi.
Aliongeza kuwa wazee ni tunu ya taifa na hivyo hawana budi kuenziwa kwa
serikali kuhakikisha kuwa wanatambuliwa na kupatiwa vitambulisho
vitakavyowawezesha kupata huduma muhimu kama vile afya.
Kwa mujibu wa Waziri Jafo wazee wanaolengwa ni wale wa kuanzia miaka 60 ambapo
inakadiriwa kuwa asilimia 75 ya wazee wote nchini wapo maeneo ya vijijini.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...