Na Greyson Mwase, Makambako
Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani amesema kuwa amefurahishwa na utekelezaji wa ujenzi wa kituo cha kupoza umeme cha Makambako kilichopo mkoani Njombe.
Kalemani aliyasema hayo leo tarehe 03 Juni, 2018 mara baada ya kukamilika kwa ziara yake katika kituo ikiwa ni sehemu ya ziara yake katika mikoa ya Njombe na Ruvuma kwa ajili ya kukagua miradi ya usambazaji wa umeme nchini inayotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO).
Alisema kuwa, mara baada ya kukamilika kwa ujenzi wa vituo vya kupoza umeme vya Makambako, Madaba na Songea mapema mwezi Septemba mikoa ya Njombe na Ruvuma itaunganishwa rasmi na Gridi ya Taifa na kuondokana na changamoto ya kukatika kwa umeme mara kwa mara.
Aliendelea kufafanua kuwa, kuingizwa kwa mikoa husika kwenye Gridi ya Taifa kutalipunguzia Shirika la TANESCO gharama kubwa inayotokana na matumizi ya mitambo ya mafuta mazito.
Katika hatua nyingine, Dkt. Kalemani alielekeza kampuni inayojihusisha na usambazaji wa umeme mkoani Njombe na Ruvuma ya Isolux kutoka Spain kuongeza kasi ya usambazaji ili wananchi waweze kupata umeme wa uhakika.
“ Haiwezekani wananchi wanakosa huduma ya nishati ya umeme wa uhakika kutokana na kusuasua kwa ukamilishwaji wa miradi ya umeme,” alisema Waziri Kalemani.
Awali akielezea utekelezaji wa mradi wa umeme wa Makambako – Songea, Meneja wa Mradi huo Mhandisi Didas Lyamuya alisema lengo la mradi lilikuwa ni kujenga njia kuu ya usafirishaji umeme wa msongo wa kV 220, yenye urefu wa kilomita 245 kutoka Makambako hadi Songea kupitia Madaba.
Meneja Mradi wa Mradi wa Umeme wa Makambako-Songea, Mhandisi Didas Lyamuya (kulia mbele) akielezea maendeleo ya ujenzi wa kituo cha kupoza umeme cha Makambako kwa Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (katikati mbele) mara alipofanya ziara katika kituo hicho Juni 03,
Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (katikati mbele) akiendelea na ziara katika kituo cha kupoza umeme cha Makambako kilichopo mkoani Njombe Juni 03, 2018
Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (mbele) akiendelea na ziara ya ukaguzi wa kituo cha kupoza umeme cha Madaba kilichopo mkoani Ruvuma.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...