Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk Hamisi Kigwangalla amezindua rasmi maonesho ya tatu ya Utalii Karibu Kusini 2018 yatakayofanyika mkoani Iringa Septemba 26 hadi 30 mwaka huu, huku akiwataka wakuu wa mikoa yote ya Nyanda za Juu Kusini kuandaa kalenda ya pamoja itakayoainisha matukio ya kimkakati katika kutangaza vivutio vya utalii katika mikoa hiyo.

Agizo hilo, Waziri Kigwangalla alilitoa mwishoni mwa wiki mkoani Songwe wakati akifunga rasmi maonesho ya utalii ya Kimondo yaliyoratibiwa kwa mafanikio makubwa na Mkoa huo huku pia akitumia fursa hiyo kuzindua rasmi Maonesho ya tatu ya Utalii Karibu Kusini 2018 yanayohusisha mikoa ya Nyanda za Juu Kusini kupitia uratibu wa mkoa wa Iringa kwa kushirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii.Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini ni Iringa,Mbeya,Songwe,Ruvuma,Njombe,Katavi na Rukwa.

Akifafanua kuhusu agizo hilo, Dk Kigwangalla alisema ipo haja ya mikoa hiyo kwa kushirikiana na Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) kuhakikisha kwamba inabuni kalenda ya pamoja itakayoainisha matukio ya kiutalii kwa kila mkoa kisha kuyapanga katika mtiririko maalumu katika kipindi cha mwaka.

"Uwepo wa kalenda ya pamoja kwenye hili utawasaidia kufahamu mkoa upi unafanya nini kwa wakati fulani na hivyo kuwa rahisi kwa mikoa jirani kuweza kutoa ushirikiano kuhakikisha tukio hilo linakuwa kubwa zaidi bila muingiliano lakini pia itatoa fursa kwa walengwa ambao ni watalii na wadau wengine kufahamu kipi kinaendelea katika ukanda huu kwa wakati husika ili na wao pia waweze kujipanga'' alifafanua.

Alisema wingi wa vivutio vya utalii katika Ukanda wa Nyanda za Juu Kusini ni sababu tosha kuweza kuvutia zaidi idadi kubwa ya watalii haswa kama mikoa hiyo itashirikiana kuvitangaza kwa pamoja kupitia matukio ya kimkakati yakiwemo maonesho ya Utalii Karibu Kusini ambayo yanafanyika mara ya tatu mkoani Iringa.
 Baada ya uzinduzi huo ikawa  ni furaha tupu!
Waziri wa Maliasili na Utalii Dk Hamisi Kigwangalla akikata utepe kuashiria uzinduzi wa maonesho ya tatu ya Utalii Karibu Kusini 2018 yatakayofanyika Septemba 26 hadi 26 mwaka huu mkoani Iringa wakati wa hafla ya ufungaji wa maonesho ya Utalii ya Kimondo yaliyohitimishwa  mkoani Songwe mwisho wiki. Wanaoshuhudia ni pamoja na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Japhet Hasunga ( wa pili kulia), Mkuu wa Mkoa wa Songwe Luteni Mstaafu Chiku Galawa (kulia kwa waziri Kigwangalla) na Mkuu wa Wilaya ya Iringa Bw Richard Kasesela (kushoto).

 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...