Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi Meja Jenerali Jacob Kingu amefanya ziara kwenye kituo Kikuu cha Uchakataji, Uzalishaji na Utunzaji wa Taarifa (Data Centre) kilichoko Kibaha mkoani Pwani na kukagua shughuli za uchakataji wa taarifa na uzalishaji wa Vitambulisho.

Pia amefanya mazungumzo na Menejimenti ya NIDA na kusisitiza umuhimu wa kuongeza kasi ya Uzalishaji kwa kuharakisha mchakato wa upatikanaji wa mitambo ya kisasa haraka ili kuongeza nguvu ya Uzalishaji kufuatia asilimia kubwa ya wananchi kukamilisha hatua ya awali ya Usajili na uchukuaji alama za kibaiolojia.

Akizungumza kwa niaba ya Kaimu Mkurugenzi Mkuu; Mkurugenzi wa Uzalishaji Ndg. Alphonce Malibiche ameeleza mpaka sasa Mamlaka imefikia hatua nzuri katika Usajili na uzalishaji wa Namba za Utambulisho na kazi kubwa iliyopo sasa ni ya uzalishaji ambao umekuwa ukienda taratibu kutokana na uwezo mdogo wa  mashine zilizopo kushindwa kuzalisha kadi nyingi kwa mara moja.

Hata hivyo amesema tayari Mamlaka ilishachukua hatua za kuagiza mashine mpya na za kisasa kusaidia kuongeza kasi ya Uzalishaji na tayari mchakato wa kumpata mzabuni umefikia hatua nzuri na pindi taratibu zitakapokamilika mashine hizo zitafungwa mara moja.

Meja Jenerali Kingu amepongeza jitihada kubwa na nzuri zinazofanywa na Mamlaka na kusisitiza umuhimu wa wafanyakazi kufanya kazi kwa uzalendo na uadilifu mkubwa huku akiielekeza Menejimenti kuangalia namna bora ya kulinda na kuongeza maslahi ya watumishi wake; ili kuongeza morali na ufanisi katika utendaji.

Mamlaka inaendelea na zoezi la kuwasajili wananchi nchi nzima na mpaka sasa imeshasajili zaidi ya wananchi mil 19.2 nchi nzima; na hadi kufikia mwezi Desemba 2018 imelenga kuwa imesajiliwa zaidi ya watanzania mil 22.
Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi Meja Jenerali Jacob Kingu  (kushoto mwenye Kaunda suti nyeupe) akisikiliza maelezo ya jinsi uchakataji wa taarifa unavyofanywa na maafisa wa NIDA alipotembelea kituo cha Uchakataji wa taarifa. Kulia ni Ndg. Alphonce Malibiche (mwenye tai nyekundu) Mkurugenzi wa Uzalishaji akitoa maelezo; na waliomzunguka ni baadhi ya wajumbe wa Menejimenti ya NIDA.

 Watumishi katika kitengo cha Uchakataji wa taarifa wakiendelea na hatua za uhakiki wa taarifa wakati wa ziara ya Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi Meja Jenerali Jacob Kingu
 Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi Meja Jenerali Jacob Kingu akikagua kazi inayofanywa na watumishi katika kituo cha Uchakataji wa Taarifa
Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi Meja Jenerali Jacob Kingu akibadilishana mawazo na Mkandarasi wa Ujenzi wa kituo cha Uchakataji wa Taarifa Kibaha Mr. Kim(Mwenye tai ya bluu), akiwa amezungukwa na wakurugenzi na wakuu wa Vitengo wa Mamlaka.
Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi Meja Jenerali Jacob Kingu katika picha ya pamoja na viongozi wa Menejimenti ya Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa inayoundwa na Wakurugenzi, Wakuu wa Vitengo na Meneja.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...