*Ni baada ya Mahakama kuwafutia dhamana baada ya kuvunja masharti

Na Karama Kenyunko blogu ya Jamii

MWENYEKITI  wa Chadema Freeman Mbowe na Mbunge wa Tarime Mjini, Ester Matiko wamepelekwa mahabusu katika gereza la Segerea ambako watakaa mpaka pale rufaa yao ya kupinga uamuzi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu itakaposikilizwa na kutolewa uamuzi.

Hatua hiyo imekuja baada ya Mbowe na Matiko kufutiwa dhamana yao dhidi ya kesi  ya uchochezi inayowakabili  pamoja na viongozi saba wa chama hicho.

Kutokana na uamuzi huo,  Wakili Peter Kibatala anayewatetea washtakiwa hao alitoa taarifa ya kukata rufaa na akaomba kupatiwa nakala ya uamuzi huo mdogo. Pia aliomba Mahakama kuahirisha kesi hiyo kusubiri rufaa watakayoifungua washtakiwa hao Mahakama Kuu itakaposikilizwa na kutolewa uamuzi kama kesi hiyo iendelee kusikilizwa

Katika uamuzi wake, Hakimu Mashauri amesema Wakili Kibatala alitoa taarifa ya kusudio la kukata rufaa chini ya kifungu cha 161 cha sheria ya makosa ya jinai sura ya 20 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

Hakimu Mashauri amesema kifungu hicho kinasema amri zote zinazotolewa ni lazima zitakatiwa rufaa mahakama Kuu kwa marejeo kufuatia taarufa hiyo, kesi hiyo imeahirishwa hadi Desemba 6 , mwaka huu kwa ajili ya kutajwa wakati wakisubiri rufaa hiyo isikilizwe na kutolewa maamuzi.

Katika rufaa yao, iliyowasilishwa chini ya hati ya dharura katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Wakili Kibatala kwa niaba ya washitakiwa  alidai kuwa wana sababu nne za kupinga uamuzi ikiwemo mahakama haijawapa nafasi wadhamini ya kujieleza kwa mujibu wa sheria.

Pia alidai Mahakama imekosea kuwafutia dhamana washitakiwa kwa sababu Novemba 12, mwaka huu Mbowe na Matiko walifika mahakamani bila kukamatwa na kuwa chini ya ulinzi.

Alidai masharti ya dhamana waliyopewa washitakiwa ni kinyume na sheria.

Mbali na Mbowe na Matiko, washtakiwa wengine Naibu Katibu Mkuu Zanzibar Salum Mwalimu na Naibu katibu Mkuu bara na Mbunge wa kibamba John Mnyika, mbunge wa Tarime Vijijini, John Heche, Mbunge wa Kawe Halima Mdee, mbunge wa bunda, Esther Bulaya, katibu Mkuu wa Chama hicho, Dk Vincent Mashinji. 

Wote kwa pamoja wanakabiliwa na mashtaka 13, ikiwemo kula njama,  kufanya mkusanyiko wenye ghasia, kuhamasisha hisia za chuki, kushawishi hali ya kutoridhika, uchochezi na kushawishi utendaji wa kosa la jinai kati ya Februari 1 na 16, 2018, Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na Mbunge wa Tarime Mjini, Ester  wakiwa tayari kupelekwa mahabusu katika gereza la Segerea ambako watakaa mpaka pale rufaa yao ya kupinga uamuzi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu itakaposikilizwa na kutolewa maamuzi.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...