Na Chalila Kibuda,Globu ya Jamii

RAIS John Pombe Magufuli kesho anatarajia kuwa mgeni rasmi katika makabidhiano ya Mfumo wa Usimamizi wa Mawasiliano ya Simu (TTMS) unaosimamiwa na Mamlaka ya Mawasiliano Nchini (TCRA), ambao pamoja na mambo mengine mfumo huo utahakiki mapato yote ya watoa huduma za mawasiliano na kugundua mawasiliano ya simu ya ulaghai.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Mhandisi James Kilaba alisema shughuli za kiuchumi zinazohusiana na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) zimeongezeka na zinaendelea kuongezeka kwa kasi nchini hivyo kunahitajika kuwepo kwa mifumo mahiri ya usimamizi kama huo. 

Amesema mfumo huo ambao ulianza kufanya kazi rasmi Oktoba mosi 2013, pamoja na mambo mengine umewezesha upatikanaji wa takwimu za mawasiliano ya simu yanayofanyika ndani na nje ya nchi pamoja na kutambua mapato na takwimu za miamala ya fedha mtandaoni. 

"Mfumo huu utawezesha kusimamia kwa ufanisi ubora wa huduma za mawasiliano na hivyo kuboresha viwango vya huduma hizo, utatambua taarifa za laini ya simu na namba tambulishi za kifaa cha mawasiliano," amesema. 

Aliongeza kuwa kazi nyingine za mfumo huo, utaweza kubaini na kufungia simu zenye namba tambulishi zilizonakiliwa pamoja na kutoa takwimu zinazohusiana na matumizi ya data na jumbe fupi. 

"Mfumo huu unaweza pia kusimamia shughuli nyingi zaidi kutokana na mazingira na mabadiliko ya teknolojia mpya zinapojitokeza aidha mfumo huo wa TTMS ni chombo muhimu kwa ajili ya maendeleo ya uchumi na kijamii nchini," amesema. 

Hata hivyo amesema katika makabidhiano hayo zaidi ya viongozi na wananchi mbalimbali ambao ni wadau wa sekta ya mawasiliano wapatao 1500 wamealikwa kuhudhuria shughuli hiyo.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Nchini (TCRA) Mhandisi James Kilaba akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na makabidhiano ya mfumo wa mawasiliano

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...