Na Zainab Nyamka, Globu ya Jamii
KATIKA kushereheka wiki ya Lugha ya Kifaransa ubalozi wa Uswizi nchini Tanzania umefanya mdahalo na wadau wa mitandao ya kijamii kwa ajili ya kufahamu changamoto wanazokutana nazo pamoja na sheria za makosa ya Kimtandao inavyotumika.
Mdahalo huo ulifanyika katika Ukumbi wa Makumbusho ya Taifa uliweza kuwakutanisha wadau mbalimbali akiwemo Wanasaikolojia, mawakili, wamiliki wa mitandao ya kijamii na jamii husika inayotumia mitandao hiyo.
Kabla ya kuanza kwa mdahalo huo, iliwekwa Filamu ya ‘The Cleaners’ iliyofanikiwa kupata tuzo ya The Geneva International Film na Forum on Human Rights kwa mwaka 2018 nchini Uswizi ambayo imekuwa inazungumzia namna mitandao ya kijamii inavyotumiwa vibaya na wale wanaohusika na kusafisha picha au video chafu wanakuwa kwenye mazingira ya aina gani.
Balozi wa Uswizi nchini Florence Tinguely Mattli amesema kuwa, filamu ya The Cleaners imeweka wazi namna watu walionyuma ya mitandao ya kijamii wanavyofanya kazi kubwa ya kuweza kusafisha yale yote ambayo hayafai kuonekana kwa jamii kimaadili au kitaaluma.
Amesema, wadau wanapokutana katika midahalo ya wazi itasaidia kwenye kubadilisha njia ya mawasiliano ikiwemo na kufahamu haki za binadamu na jinsi mitandao ya kijamii inavyoweza kubadilisha maisha ya watu ikiwemo Kutoa elimu kwa nchi ya Tanzania.
“Kuna kazi kubwa inafanywa na wasafishaji walio nyuma ya maudhui mbalimbali ya Mitandao ya Kijamii na wanakutana na picha za aina tofauti kwa siku na wanazifuta na hilo linasaidia kulinda maadili ndani ya jamii”, amesema Mattli.
Mmiliki na Mwanzilishi wa Jamii Forum Maxence Melo amesema kuwa watu wamekuwa wanatumia mitandao ya kijamii vibaya na hata kwa nchini kwetu namna wanavyopambana kulinda maudhui ya Kiswahili kama kinachofanyika kwenye filamu ya The Cleaners.
Maxence amesema, watumiaji wa zamani wa mitandao walikuwa ni wasomi na kabla ya kuiweka mtandaoni wanafikiria maudhui ila kwa sasa hivi watumiaji wa mktandao ya kijamii wamekuwa wengi na kila mmoja anaweka kile anachojisikia kwa muda huo.
Mwanasaikilojia Araika Mkulo amesema, filamu ya the Cleaners imeonesha kiasi gani walio nyuma ya mitandao ya kijamii wanapata changamoto kubwa sana ukilinganisha na namna watu wanavyofikiria. “Takribani kwa siku mtu anakutana na picha zisizo na maadili 25,000 na kujiuliza je wanapata stahiki zao kama inavyotakiwa kwani wamekuwa wanakutana na changamoto za kisaikilojia kutokana na kuona picha chafu na zisizo na maadili mara kwa mara,”amesema .
Wakili wa kujitegemeaBenedict Ishabakaki amesema kwa serikali ya Tanzania imeweka sheria ya makosa ya kimtandao Kipengele cha 12 kikielezea adhabu ya mtu atakayeweka picha au taarifa isiyo na maadili kwenye mtandao wa kijamii ambapo anaweza kufungwa kifungo kisichopungua mwaka mmoja au faini isiyopungua Milion 5 au vyote kwa pamoja.
Filamu ya The Cleaners inaonesha namna jamii inavyotumia mitandao ya kijamii pasi na kufuata maudhui au maadili na watu walionyuma ya mitandao hiyo wakiwa wanafanya jitihada za kusafisha picha chafu na zisizo kwa dunia nzima.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...