NA SULEIMAN MSUYA

MRADI wa Kuleta Mageuzi Katika Sekta ya Mkaa Tanzania (TTCS) maarufu 'mkaa endelevu' umefanikiwa kuingizia halmashauri, vijiji na wananchi zaidi ya shilingi bilioni 3 kuanzia 2014 hadi sasa.

Hayo yamesemwa na Meneja Mradi wa TTCS, Leonard Charles wakati akiwasilisha mada kwa maofisa mbalimbali kutoka Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Serikali Kuu walikutana mkoani Morogoro.

Meneja huyo amesema mradi wa TTCS unatekelezwa katika vijiji 30 vya wilaya za Mvomero, Kilosa na Morogoro chini ya usimamizi wa Shirika la Kuhifadhi Misitu ya Asili Tanzania (TFCG), Mtandao wa Jamii wa Kusimamia Misitu Tanzania (Mjukita), Shirika la Kuendeleza Nishati Asili Tanzania (TaTEDO) na kufadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Uswisi (SDC).

Amesema katika mradi huo vijiji 22 vimeanza kunufaika katika pande mbili ambazo ni kiuchumi na utunzaji wa mazingira huku nane vikiwa katika mchakato.

Ameongeza hadi kufikia mwezi Mei 2019 vijiji vimeweza kikusanya mapato halali zaidi ya shilingi bilioni 1.4, wachomaji mkàa shilingi bilioni 1.2 na halmashauri shilingi milioni 500.

Ametaja baadhi ya vijiji ambavyo vimenufaika na mradi ni Ulaya Mbuyuni, Matuli, Kitunduweta, Mlilingwa, Ulaya Kibaoni, Diguzi na vingine.

Leonard amesema mradi wa mkaa endelevu ulianza Machi 2012 katika vijiji 10 lakini baada ya kuonekana mafanikio wamelazimika kuongeza vijiji hadi kufika 30.

"Mradi wa TTCS maarufu mkaa endelevu umefanya mapinduzi makubwa kiuchumi, kijamii na maendeleo katika vijiji vilivyopo kwenye mradi kama kuboresha sekta ya afya, elimu, maji, kilimo na mitaji," amefafanua.

Ameongeza mafanikio ya mradi yamezingatia kutoa elimu kwa jamii husika, watendaji na wafanya maamuzi hivyo kurahisisha utekelezaji.

Amesema pia utekelezaji unazingatia uwepo wa mpango wa matumizi bora ya ardhi za vijiji, kutenga maeneo madogo ya mradi na kuvuna kwa kutumia vitalu.Pia mradi umefanikisha ujenzi wa ofisi za vijiji hali ambayo inarahisisha usimamizi wa mradi.

Kwa upande wake Ofisa Uhusiano wa TFCG, Bettie Luwuge amesema warsha hiyo ya siku tatu imelenga kujenga uelewa kwa pande zote ili kurahisisha utunzaji wa misitu nchini.

Luwuge amesema rasilimali misitu ikitunzwa kwa ushirikiano wa wadau wote inaweza kubadilisha jamii kiuchumi na maendeleo.

"Tumeamua kukutanisha maofisa kutoka sekta ya kilimo, misitu, maliasili na sheria wa wilaya 19 lengo ni kuweza kubadilishana mawazo namna ya kutunza misitu yetu ili iwe endelevu," amesema.

Amezitaja  wilaya husika kwa warsha hiyo ni Kigoma, Kilwa, Tabora, Namtumbo, Handeni, Kilindi, Mvomero, Morogoro, Kilosa, Lindi, Liwale, Tunduma, Kilolo, Ruangwa, Nachingwea, Mpwapwa, Songea, Nyasa, Mbinga.

Awali akifungua warsha hiyo Ofisa Misitu wa Mkoa wa Morogoro, Joseph Chuwa alisema warsha hiyo itasaidia kuongezea uelewa maofisa hao kuhusu utunzaji misitu ya vijiji.

Chuwa alisema rasilimali mali misitu ikitunzwa kwa dhana ya uendelezaji itasaidia jamii kuinuka kiuchumi.
Meneja Mradi wa TTCS, Charles Leonard akitoa mada kuhusu Mkaa endelevu  kwa maofisa mbalimbali kutoka wilaya 19 nchini.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...