Na Karama Kenyunko, Michuzi Tv
RAIA wa Hungary Akos Berger (28), amepandishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na mashitaka ya kusafirisha dawa za kulevya zenye uzito wa gramu 250 aina ya Amphetamine.
Berger amefikishwa mahakamani hapo leo Juali 25,2019 na kusomewa mashitaka mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi Maira Kasonde.
Akisoma hati ya mashtaka, Wakili wa Serikali, Grory Mwenda amedai, Julai 19 mwaka huu, eneo la Mbezi Beach jijini Dar es Salaam, mshtakiwa alitenda kosa hilo.
Hata hivyo, baada ya kusomewa mashitaka hayo, Hakimu Kasonde alimtaka mshitakiwa kutojibu chochote kwa kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi ya dawa za kulevya, usipokuwa kwa kibali maalumu kutoka kwa DPP
Upande wa mashitaka umedai upelelezi wa kesi hiyo haujakamilka na kesi iliahirishwa hadi Agosti 9 mwaka huu itakapotajwa.
Wakati huo huo, Wafanyabiashara wawili wa jijini Dar es Salaam wamefikishwa mahakamani hapo wakikabiliwa na mashitaka ya kusafirisha dawa za kulevya zenye uzito wa kilogramu 21.67.
Wakili wa Serikali, Daisy Makakala amewataja washitakiwa hao kuwa ni Ramadhan Gumbo (25) mkazi wa Ilala na Fahad Salehe (24).
Makakala amedai mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi kuwa Julai 13, mwaka huu maeneo ya Mbezi wilayani Kinondoni, walisafirisha dawa za kulevya aina ya Heroin Hydrochloride.
Hakimu Shaidi amewataka washitakiwa kutojibu chochote kwa sababu mahakama hiyo haina mamlaka.
Kwa mujibu wa upande wa mashtaka upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika na Hakimu Shaidi ameahirisha kesi hiyo hadi Agosti 9, mwaka huu kwa ajili ya kutajwa na washitakiwa wamerudishwa rumande.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...