Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 27 Novemba, 2019
amepiga marufuku halmashauri zote za Majiji, Manispaa, Miji na Wilaya hapa
nchini kukopa fedha za kutekeleza miradi kutoka benki, na badala yake ameagiza miradi
hiyo itekelezwe kwa kutumia fedha za bajeti na mapato ya ndani ya halmashauri
hizo.
Mhe. Rais Magufuli
ametoa agizo hilo wakati akiwasalimu wananchi wa Ushirombo katika Wilaya ya
Bukombe Mkoani Geita akiwa safarini kutoka Dodoma kwenda Chato Mkoani Geita.
Kabla ya
kuwasalimu wananchi hao, Mhe. Rais Magufuli amesalimiana na wananchi wa Kahama
Mkoani Shinyanga ambapo Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji huo Bw. Anderson David
Msumba amemueleza kuwa halmashauri hiyo imekopa shilingi Bilioni 8 kwa ajili ya
kujenga kituo cha mabasi.
Mhe. Rais Magufuli
amemtaka Mkurugenzi huyo kuachana na mkopo huo na amepiga marufuku halmashauri
zote nchini kwenda kukopa benki fedha za kutekeleza miradi, na kwa ambazo
zimeshakopa kurejesha fedha hizo vinginevyo Wakurugenzi wa halmashauri hizo
wataondolewa katika nyadhifa hizo.
Amefafanua kuwa mamlaka
ya kukopa fedha za miradi ya Serikali yapo mikononi mwa Katibu Mkuu wa Wizara
ya Fedha na Mipango na sio kila halmashauri kukopa inavyotaka tena kwa riba
kubwa kwa kuwa mwishowe Watanzania wote ndio watakaowajibika kuilipa kupitia
hazina.
Akiwa katika
safari hiyo Mhe. Rais Magufuli amewahakikishia wananchi wa Igunga, Nzega,
Tabora pamoja na maeneo yote yaliyopangwa kupitiwa na mradi wa maji kutoka Ziwa
Victoria kuwa matatizo ya maji yanayowakabili wananchi hao yatakwisha baada ya
mradi huo kukamilika.
Mhe. Rais Magufuli
amesema mradi huo ambao utagharimu shilingi Bilioni 620 hadi kukamilika upo
katika hatua za ujenzi na mara maji yatakapofikishwa katika maeneo hayo
Serikali itahakikisha yanasambazwa kwa wananchi.
Kabla ya kufika
Igunga, Nzega na Tabora, Mhe. Rais Magufuli amesalimiana na wananchi wa Shelui
Mkoani Singida ambapo amemuagiza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa
na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo kutoa shilingi Milioni 250 kwa ajili ya
ujenzi wa kituo cha afya cha Shelui ifikapo Januari 2020, baada ya wananchi hao
kuomba wasaidiwe kujengewa Kituo cha Afya kama walivyoahidiwa miaka ya nyuma.
Mhe. Rais Magufuli
amewapongeza wananchi wa maeneo hayo pamoja na maeneo mengine ya Isaka, Kahama,
Masumbwe, Uyovu Runzewe na Bwanga kwa mabadiliko makubwa ya kimaendeleo na
amewahimiza kuendelea kuchapa kazi za uzalishaji mali hasa wakati huu ambapo
mvua zinanyesha ili kujihakikishia chakula na kipato zaidi kutokana na kilimo.
Amesema Serikali
ya Awamu ya Tano imechukua hatua mbalimbali za kupigania maslahi ya Watanzania ikiwemo
sekta ya madini ambapo pamoja na kuwatetea wachimbaji wadogo imetunga sheria ya
kuhakikisha nchi inanufaika na rasilimali hiyo, na katika hilo ameipongeza
kampuni ya dhahabu ya Barrick kwa kukubaliana na Serikali kuunda kampuni ya
pamoja iitwayo Twiga ambapo Serikali itakuwa inapata faida kwa asilimia 50 na kampuni
ya Barrick itapata asilimia 50.
Akiwa Kahama, Mhe.
Rais Magufuli amewasikiliza akina Mama watatu waliokuwa wakidai kudhurumiwa
haki zao ambapo ameagiza Askari Polisi (Koplo
Pascal Edward) anayedaiwa kusababisha kifo cha
Mme wa Evanis Raymond Mzare baada ya kumgonga na gari, kusimamishwa kazi mara
moja na hatua za kijeshi kuchukuliwa dhidi yake kutokana na kudaiwa kufanya
njama za kuharibu kesi inayomkabili.
Pia amemuagiza Kaimu
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Shinyanga ACP
-
Sofia Jongo kumkamata mtu aitwaye Daudi anayedaiwa kumpiga hadi kumvunja mkono
Mama aitwaye Maria Mavita wakati akifanya kazi zake za kuponda kokoto na
amemuagiza Afisa Ardhi wa Halmashauri ya Mji wa Kahama Bw. Clement Mkusa
kufuatilia kesi ya Mama aitwaye Joyce Lenard anayedai hati ya nyumba yake
imeghushiwa na kuna njama zinafanyika kumpora nyumba hiyo.
Gerson
Msigwa
Mkurugenzi
wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Chato
27 Novemba,
2019
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...