NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar 
Dk.Abdulla Juma Mabodi,akifungua Kongamano la Wiki ya Kachorora la 
kuadhimisha miaka 20 toka kuanzishwa kwa Maskani ya CCM ya Kachorora 
iliyopo Mwembe Shauri Zanzibar. 
 
 
 
AFISA Mwandamizi kutoka Afisi Kuu 
ya UVCCM Zanzibar Ndugu Shara Ame Ahmed, akitoa mada ya dhana ya 
kuanzishwa kwa Maskani, katika kongamano la wiki ya Kachorora 
lililofanyika katika ukumbi wa Kituo cha kulelea Wazee Sebleni Zanzibar. 
 
 
 
MJUMBE wa Maskani ya Kachorora 
Ndugu Suleiman Omar ‘Ganzi’ akitoa nasaha juu ya umuhimu wa Wanachama wa
 CCM kuwarithisha Watoto itikadi na fikra za ukombozi kabla na baada ya 
Mapinduzi ili wakue wakijua historia halisi ya nchi.

NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar 
Dk.Abdulla Juma Mabodi,akiwa na Wana Maskani ya Kachorora pamoja na 
Maskani mbali mbali zilizoalikwa katika hafla hiyo, wakifuatilia kwa 
makini mada mbali mbali zinazowasilishwa katika kongamano hilo la Wiki 
ya Kachorora, lililofanyika ukumbi wa Sebleni Wilaya ya Amani kichama 
Zanzibar.
***********************************
NA IS-HAKA OMAR,ZANZIBAR.
NAIBU Katibu Mkuu
 wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) Zanzibar Dk.Abdulla Juma Mabodi,amesema 
siasa za ulaghai na uchochezi wa vurugu zinazofanywa na upinzani 
visiwani Zanzibar, hazitozuia ushindi wa CCM katika Uchaguzi Mkuu wa 
mwaka 2020.
Amesema  Chama 
cha Mapinduzi kitapata ushindi wa kihistoria kwa majimbo ya Unguja na 
Pemba ambao haujawahi kutokea toka kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi 
nchini mwaka 1992.
Kauli hiyo 
ameitoa wakati akifungua kongamano la wiki ya Kachorora lililofanyika 
katika ukumbi wa Kituo cha kulelea Wazee Sebleni Wilaya ya Amani kichama
 Zanzibar.
Alisema ushindi 
huo utapatikana kutokana na utekelezaji mzuri wa Ilani ya CCM ya mwaka 
2015/2020 kwa wananchi wote mijini na vijijini , ambao kila mwananchi 
kwa sasa ananufaika na huduma muhimu za kijamii zilizoimarishwa na 
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Alieleza kuwa 
hakuna chama cha siasa chochote duniani kilichopata kibali na ridhaa ya 
kuongoza dola kupitia njia ovu za vurugu,vitisho na uongo badala yake 
vyama vinavyoongoza dola ni vile vilivyokuwa karibu na wananchi kutokana
 na uhodari wa kutekeleza kwa vitendo matakwa ya wananchi.
Dk.Mabodi, 
alifafanua kuwa CCM itaendelea kuweka vipaumbele vya kuisimamia serikali
 itekeleze kwa vitendo sera za maendeleo kwa wananchi,huku wapinzani 
wakiendelea kujinadi na kupiga porojo zisizokuwa na tija kwa wananchi.
“Chama cha 
Mapinduzi hakitishwi na hakiogopi taasisi yoyote ya kisiasa wala kundi 
la watu , kwani ni chama imara na chenye historia kubwa barani Afrika na
 Duniani kote hivyo hao walioanza kujitokeza kuleta uchochezi tunawaonya
 waache kuchafua nchi vinginevyo watajuta kwa uovu wao.
Nawambia kwamba 
ushindi wetu ni lazima kama Ibara ya 5 ya Katiba ya CCM ya mwaka 1977 
toleo jipya la 2017 inavyoelekeza, sasa tuwaone na uchaguzi huu watakuja
 na uongo upi kwani uchaguzi uliopita waliiba kura na kuvuruga uchaguzi 
na uchaguzi wa marudi wakasusia.”,alisema Dk.Mabodi.
Kupitia kongamano
 hilo alivitaka vyombo vya Ulinzi na Usalama nchini kutekeleza wajibu 
wao kwa kudhibiti uvunjifu wa amani na utulivu, ulioanza kuvunjwa na 
baadhi ya wanasiasa wanaotamka kauli za uchochezi bila kuchukuliwa hatua
 za kisheria.
Alisema Chama cha
 Mapinduzi kwa muda mrefu kimekuwa na uvumilifu wa kisiasa kwa kuheshimu
 sheria,miongozo na kanuni za Uchaguzi na nchi lakini hakitokuwa tayari 
kuona baadhi ya wanasiasa wanaibuka na kuhamasisha vurugu.
“Itafikia wakati 
uvumilivu wetu utakuwa na kikomo kama vyombo vya ulinzi na usalama 
mtashindwa kuwadhibiti hao wanaofanya vurugu wakiweka mguu wa kushoto na
 sisi tutaweka mguu wa kulia, nchi haitakalika na hatutaki kufikia huko 
bali tushindane kwa hoja na sera za kimaendeleo.”, alisisitiza Naibu 
Katibu Mkuu huyo.
Aliwambia 
wanachama wa CCM walioshiriki katika Kongamano hilo kuwa wanatakiwa 
kuwahamasisha wananchama wenzao na wananchi kwa ujumla kujitokeza kwa 
wingi kushiriki katika zoezi la uandikishaji wa daftari la wapiga kura 
linalotarajiwa kuanza Januari 18 kisiwani Pemba.
Alisema ushiriki 
wa Wana CCM katika zoezi hilo la Daftari la wapiga kura ni sehemu muhimu
 ya kuandaa mazingira ya ushindi wa CCM kwani ndio chimbuko la 
kupatikana wapiga kura watakaofanikisha ushindi wa CCM uchaguzi mkuu 
ujao.
Katika maelezo 
yake Dk.Mabodi,aliwataka Wabunge, Wawakilishi na Madiwani kufanya 
mikutano ya Hadhara katika maeneo yao na kueleza kwa kina namna  
walivyotekeleza Ilani ya CCM ya mwaka 2015/2020.
Akizungumzia 
umuhimu wa maskani Dk.Mabodi, alisema maskani ni sehemu ya kueneza 
itikadi na kupanga Mapinduzi ya kiuchumi yenye kuleta maendeleo 
endelevu.
Alisema viongozi 
namba moja ndani ya Chama cha Mapinduzi ni mabalozi wa mashina na 
maskani hivyo ni lazima viongozi washuke katika ngazi hizo kufahamu 
mahitaji yao na kupokea ushauri wa kujenga chama.
Aliwapongeza Wana
 Maskani ya kachorora kwa ubunifu wao wa kuandaa kongamano la kujadili 
masuala muhumu ya kujenga chama sambamba na kuzialika maskani zingine 
ili kuendeleza umoja na mshikamano.
“Maskani ya 
kachorora ni kati ya maskani kubwa tatu Tanzania zilizofanya mambo 
makubwa nchini na zenye historia ya chimbuko la kueneza itikadi na 
miongozo imara ndani nan je ya chama chetu”, alisema.
Dk.Mabodi, 
aliwapongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi 
Dk.Ali Mohamed Shein pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania 
Dkt.John Pombe Magufuli kwa uchapakazi wao mzuri
Naye Katibu wa 
Maskani ya Kachorora ndugu Samia Leonard Shirima,alisema lengo la 
kufanya kongamano hilo ni kutoa elimu ya juu ya masuala mbali mbali 
yanayotekezwa na CCM pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Aidha,alisema 
makani hiyo inasherehekea miaka 20 toka kuanzishwa kwake hivyo inafanya 
shughuli mbali mbali za kijamii zikiwemo kufanya usafi,kutembelea 
viongozi wastaafu na wazee wa Chama cha Mapjnduzi.
Katika kongamano 
hilo la siku moja zilizotolewa mada tatu zikiwemo unyanyasaji wa 
kijisia, dhana ya kuanzishwa kwa maskani pamoja na Mafanikio ya awamu ya
 saba.


 

Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...