Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maji,
Mhandisi Anthony Sanga (katikati) akikagua ujenzi wa mradi wa maji wa
Orukesment Wilayani Simanjiro wakati wa ziara yake kwenye mradi.
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maji,
Mhandisi Anthony Sanga (wa pili kushoto) akikagua ujenzi wa mradi wa
maji wa Orukesment Wilayani Simanjiro wakati wa ziara yake kwenye mradi.
Kushoto ni mwakilishi wa Kampuni ya Jandu Plumbers, Mhandisi Kotturu
Ramnadh.
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maji,
Mhandisi Anthony Sanga (kushoto) akitoa maelekezo kwa Mkandarasi Jandu
Plumbers kuhusiana na uekelezaji wa mradi wa maji wa Orukesment Wilayani
Simanjiro. Katikati ni mwakilishi wa Mkandarasi, Kotturu Ramnadh.
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maji,
Mhandisi Anthony Sanga (katikati) akikagua ujenzi wa mradi wa maji wa
Orukesment Wilayani Simanjiro wakati wa ziara yake ya kukagua hatua ya
ujenzi wa mradi.
**************************
NAIBU Katibu Mkuu
Wizara ya Maji Mhandisi Anthony Sanga amemtaka Mkandarasi Jandu
Plumbers wa Arusha anayejenga mradi wa Maji wa Orukesment Wilayani
Simanjiro kuukamilisha kwa muda uliyopangwa.
Ametoa
maelekezo hayo Desemba 14, 2019 alipotembelea na kukagua maendeleo ya
ujenzi wa mradi huo Wilayani Simanjiro sambamba na kuzungumza na
mkandarasi.
Akiwa katika
ukaguzi wa utekezaji wa mradi, Mhandisi Sanga alibaini shughuli
zinazoendelea kutekelezwa na Mkandarasi kuegemea zaidi maeneo ambayo
hayapelekei wananchi kupata huduma ya maji mapema iwezekanavyo kama
ilivyo dhamira ya Serikali.
Alibainisha
kwamba Mkandarasi anajenga maeneo ambayo siyo kipaumbele cha mradi na
hivyo alimtaka kuhakikisha anaelekeza nguvu zaidi kwenye ujenzi wa
maeneo yatakayowapatia wananchi maji ikiwemo ujenzi wa chanzo, kituo cha
tiba ya maji na bomba kuu la kusafirishia maji.
”Nilichokiona
hapa kwenye mradi ni kwamba Mkandarasi amejikita zaidi katika kujenga
majengo ya ofisi na nyumba za wafanyakazi ambayo hayapelekei wananchi
waanze kupata maji badala ya kujielekeza kwenye maeneo yenye tija ya
kuleta huduma ya maji kwa haraka ili wananchi waanze kunufaika,” alisema
Mhandisi Sanga.
Mhandisi
Sanga alifafanua kwamba mradi wa maji katika Mji wa Orukesment unao
umuhimu mkubwa kwa wananchi wa maeneo hayo hasa ikizingatiwa kuwa
umekuwa ukisubiriwa kwa muda mrefu.
“Wananchi
wameusubiri sana huu mradi, wamekuwa na shauku kubwa ya kuanza kupata
huduma kutoka hapa, sijaridhishwa na huu utaratibu anaoendelea nao
Mkandarasi, ningependa kuona matokeo ya haraka kutoka hapa,” alisisitiza
Mhandisi Sanga.
Awali
akiwasilisha taarifa ya maendeleo ya ujenzi wa mradi huo kwa Mhandisi
Sanga, Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira
Babati (BAWASA), Mhandisi Iddi Msuya ambao ndio wasimamizi wa mradi
huo alieleza tayari wamemuagiza Mkandarasi kuhakikisha anaongeza nguvu
kazi ili kutekeleza maeneo nyeti kwa haraka zaidi.
Alibainisha
kuwa kukamilika kwa mradi kutanufaisha zaidi ya wakazi 52,000 na mifugo
katika mji wa Orkesumet pamoja na vijiji vinavyozunguka mji huo.
Mhandisi
Msuya alimuahidi Naibu Katibu Mkuu Sanga kuhakikisha anasimamia vyema
maelekezo aliyotoa ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma mapema
iwezekanavyo. Kwa upande
wake mwakilishi wa Kampuni ya Jandu Plumbers, Mhandisi Kotturu Ramnadh
aliahidi kukamilisha ujenzi wa mradi huo katika kipindi kilichowekwa cha
mwezi Aprili, 2020.
Aidha
aliahidi kuongeza nguvu katika ujenzi wa chanzo na kituo cha tiba ya
maji sambama na bomba kuu la kusafirisha maji kama ilivyoelekezwa na
Naibu Katibu Mkuu Sanga.
Mradi wa maji
Orukesment unatekelezwa na Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na
Benki ya Maendeleo ya Nchi za Kiarabu kwa nchi za Afrika (BADEA) na
Mfuko wa Maendeleo wa nchi zinazozalisha mafuta (OFID) kupitia mkopo wa
masharti nafuu ambao umetengewa jumla ya Dola za Marekani Milioni 18.42
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...