Katibu wa ALAT Taifa, Elirehema Kaaya akipata maelezo kutoka kwa mtaalamu wa uchakataji wa zabibu kutoka kiwanda cha UWAZAMAM kilichopo kata ya Mpunguzi jijini Dodoma baada ya kamati ya utendaji ya Jumuiya hiyo kufanya ziara ya kukagua maendeleo yake.
Mmoja wa vijana ambao ni wataalamu wa uchakataji wa zabibu kutoka kiwanda cha UWAZAMAM akitoa maelezo ya namna zoezi hilo linavyofanyika kwa kamati ya utendaji ya ALAT Taifa iliyofika kiwandani hapo kukagua maendeleo ya kiwanda hicho.
Makamu Mwenyekiti wa ALAT Taifa, Stephen Mhaga akizungumza baada ya kukagua kiwanda cha kuchakata zabibu cha UWAZAMAM kilichopo kata ya Mpunguzi jijini Dodoma..
Vijana ambao ni wataalamu wa uchakataji wa zabibu kutoka kiwanda cha UWAZAMAM wakiendelea na zoezi lao la uchakataji.
Kamati
ya Utendaji ya ALAT Taifa ikiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa
kiwanda cha kuchakata zabibu cha UWAZAMAM kilichopo kata ya Mpunguzi
jijini Dodoma.
Charles James, Michuzi TV
KAMATI ya utendaji ya Jumuiya ya Tawala za Mitaa (ALAT) nchini Taifa imefanya ziara katika kiwanda cha kuchakata zabibu Uwazamam kilichopo katika eneo la Mpunguzi jijini Dodoma kujionea shughuli za uendashwaji wake.
Kiwanda hicho ambacho kilianzishwa kwa msaada wa ALAT kimekua kikichakata zabibu yake na kuuza mchuzi wa zabibu kwa makampuni makubwa yaliyopo ndani ya Dodoma na nje ya Jiji hilo.
Akizungumza na watumishi wa kiwanda hicho, Makamu Mwenyekiti wa ALAT Taifa, Stephen Mhaga amesema Jumuiya yake itaendelea kushirikiana na vikundi vinavyomiliki viwanda hivyo katika kuwatafutia mitaji, kuwapa elimu na fursa za kujiwezesha.
Amesema ni jambo la kujivunia kuona kiwanda hicho kinavyofanya kazi zake huku kikikua siku hadi siku na hivyo kuendana na sera ya awamu ya tano ya kufikia uchumi wa kati kupitia viwanda.
" Niwapongeze sana. Pamoja na changamoto mbalimbali zilizopo lakini mnafanya jambo kubwa ambalo lina manufaa kwenu, wakulima wa zabibu ambao wamekua wakifanya biashara na nyinyi na zaidi lina manufaa pia kwa serikali yetu katika kukuza uchumi wa Nchi.
Tunawaahidi kushirikiana na nyingi katika kuwapatia ufadhili kutoka kwa wadau mbalimbali wa maendeleo kama tulivyofanya awali kwa kuwaunganisha na wafadhili wengine kama LIC lakini ombi langu kwenu ni kuwaona mnakua kutoka hapa mlipo," Amesema Mhaga.
Kwa upande wake Katibu Mkuu wa ALAT Taifa, Elirehema Kaaya ameupongeza uongozi wa chama hicho cha ushirika kwa namna kinavyozidi kukua ikiwa ni pamoja na kuongeza idadi ya wanachama wake kutoka 50 hadi 196.
Amesema akiwa kama Mtendaji Mkuu wa ALAT atahakikisha chama hicho linaendelea kukua kutoka kuwa wachakataji wa zabibu pekee yake na kuwa kiwanda kikubwa ambacho kitakua kinazalisha mvinyo na siyo kuuza mchuzi kwa makampuni makubwa.
" Sisi lengo letu ni kuona mnapiga hatua. Hapa mlipofikia inatosha na sasa mnapaswa kuwa kiwanda kikubwa zaidi. Kama Jumuiya ya Tawala za Mitaa tutaendelea kushirikiana na nyinyi kuhakikisha malengo yenu yanatimia," Amesema Kaaya.
Awali akisoma taarifa ya chama hicho, Meneja wa UWAZAMAM, Bakari Mavula ameishukuru ALAT kwa namna ambavyo wamekua msaada kwao katika ukuaji wa kiwanda chao hicho hasa katika gharama za umaliziaji wa jengo lao, miundombinu ya umeme na maji pamoja ba kutoa mafunzo kwa wakulima.
Amesema kupitia kiwanda hicho wakulima wa kata hiyo ya Mpunguzi wameweza kunufaika kwa kupata soko la uhakika la zabibu yao tofauti na miaka ya nyuma ambapo asilimia 30 ya zabibu ilikua inaharibikia mashambani kwa kukosa soko.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...