Katika kuunga mkono juhudi za Serikali za kudhibiti taka za plastiki, Kampuni ya Coca-Cola Kwanza imezindua kampeni inayofahamika kama Tanzania Bila Taka.

Lengo la kampeni hii ni kuelimisha, kushirikisha umma na kujenga mabadiliko ya tabia kupitia Coca-Cola Kwanza ambayo imekuwa na mwendelezo wa utaratibu wa kuleta mabadiliko katika utunzaji wa mazingira kupitia kampeni zake za Mchanga Pekee, Cash for Trash (Fedha kwa taka) na COPA Coca-Cola Rejesha na Ushinde.

Uzinduzi wa Kampeni hiyo umefanyika kwa namna ya kipekee, ambapo Coca-Cola Kwanza imetumia mabasi 10 ya Mwendokasi kubeba ujumbe wa kampeni hiyo ya Tanzania bila Taka katika hafla iliyofanyika katika ofisi za UDART jijini Dar es Salaam leo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkurugenzi wa Mahusiano kwa Umma na Mawasiliano Coca-Cola Kwanza, Haji Ally Mzee alisema, kampeni hiyo inaambatana na mpango wa Kimataifa wa Kampuni ya Coca-Cola duniani uliopewa jina la dunia bila taka. Kampeni inakusudia kubuni namna bora zaidi ya kurejesha chupa za plastiki, kuongeza makusanyo kwa kushirikisha jamii, Taasisi na hata washindani wake ili kupunguza tatizo hilo.

“Kama kampuni tunatambua hatari ambayo plastiki inaweza kusababisha ikiwa hakuna mtu wa kushughulikia tatizo la taka. Hivyo basi tunapotambua juhudi za Serikali katika kushughulikia taka za plastiki, tuliona nasi tuna wajibu wa kuchangia kuifanya nchi yetu isiwe na taka,”alisema.

Haji alitoa wito kwa watanzania kujijengea tabia ya kuziondoa taka zinazozagaa hovyo hasa chupa za plastiki ambazo hujaa barabarani, kwenye mifumo ya maji na maeneo ya umma.

Alisema pia, katika juhudi za kukuza uchumi mviringo wa Tanzania, Coca-Cola Kwanza inashirikiana na Kampuni ya Sunda Fiber katika kutengeneza vifaa vya nyuzi na kamba kutoka kwenye chupa za plastiki zilizokusanywa.

Kwa upande wake, Afisa Mahusiano na Mawasiliano kwa Umma wa Coca-Cola Kwanza, Victor Byemelwa alisema, “Mwaka huu, mpango tulionao ni kuendeleza Kampeni yetu katika mikoa mingine ya Tanzania kama Dodoma, Mbeya, Mtwara na mingine mingi. Pia kwa kila robo mwaka tutaendesha Kampeni yetu ya Cash for Trash (Fedha kwa Taka) kwa kuendelea kuishirikisha jamii”.

Victor aliongeza kuwa, mwaka jana, Kampeni ya Coca-Cola COPA Rejesha na Ushinde ulipokelewa vema na vijana walioshiriki katika mashindano ya mpira wa miguu ya COPA Coca-Cola.

“Kupitia shule hizi, tulifanikiwa kukusanya idadi kubwa zaidi ya kilo 880,835.05 (tani 880). Ninaamini, kupitia kampeni hii tuliweza kushawishi mabadiliko ya tabia miongoni mwa vijana na tunatarajia kuendelea na mwenendo huo mwaka huu,”alisema Victor.

Pia aliongeza kuwa, mwaka huu wanatarajia kufunga vifaa vya taka katika vyuo na baadhi ya maeneo ya umma ikiwa ni sehemu ya mipango ya kudhibiti taka ya kampuni hiyo.

Mwaka 2019, Kampuni ya Coca-Cola na washirika wake wanaotengeneza Soda za kampuni hiyo walianza mipango kadhaa ya kusaidia kumaliza changamoto ya taka za plastiki kwa kuratibu Kampeni kadhaa ikiwemo COPA Coca-Cola Rejesha na Ushinde, Mchanga Pekee kwa ajli ya usafi wa fukwe na taka kwa fedha.

Hatua hizi zilikusanya chupa zote bila kujali ni vifungashio vya Coca Cola pekee. Mwisho wa mipango kampuni ilifanikiwa kukusanya plastiki milioni 40, kiwango ambacho wangependa kukivuka mwaka huu.
Mkurugenzi wa Mahusiano kwa Umma na Mawasiliano Coca-Cola Kwanza, Haji Ally Mzee (katikati) akifafanua jambo kwa Mkurugenzi Mtendaji wa UDART, John Nguya (kushoto) wakati wa hafla ya uzinduzi wa kampeni ya Tanzania Bila Taka iliyozinduliwa na Kampuni hiyo katika ofisi za UDART jijini Dar es salaam mwishoni mwa juma. Kampuni ya Coca-Cola Kwanza imeamua kuyatumia mabasi ya mwendokasi kubeba ujumbe wa Kampeni yake wenye lengo la kuelimisha, kubadili tabia na kushirikisha umma katika kutunza mazingira. Kulia ni Afisa Mahusiano kwa Umma na Mawasiliano Coca-Cola Kwanza, Victor Byemelwa.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...