Jumla ya wagonjwa 12 ambao mishipa yao ya damu ya moyo imeziba kwa muda mrefu (Total Chronic Occlusion - CTO) wanatarajiwa kufanyiwa upasuaji unaohitaji utaalamu wa hali ya juu katika kambi maalum ya matibabu inayofanyika katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).

Akizungumza na waandishi wa habari  leo jijini Dar es Salaam Daktari mbobezi wa moyo na mzibuaji wa mishipa ya damu ya moyo wa JKCI Peter Kisenge alisema kambi hiyo ya siku tatu wanaifanya kwa kushirikiana na daktari  kutoka nchini Saud Arabia na  Shirika la Madaktari Afrika la nchini Marekani.

“Matibabu ya wagonjwa ambao mishipa yao ya damu imeziba na kukaa kwa muda mrefu bila ya kupata matibabu ni magumu na yanahitaji utaalamu wa hali ya juu. Kupitia kambi hii  wagonjwa wenye matatizo hayo watapata matibabu”, alisema Dkt. Kisenge.

Dkt. Kisenge ambaye pia ni Mkurugenzi wa Tiba ya Moyo alisema aina ya matibabu yanayofanyika ni ya kuzibua mishipa ya damu ya moyo kwa njia ya upasuaji mdogo wa moyo wa bila kufungua kifua kwa kutumia mtambo wa Cathlab (Catheterization Laboratory) ambapo mgonjwa anatobolewa tundu dogo katika mshipa wa damu wa mkono.

“Upasuaji wa aina hii una faida kubwa kwa mgonjwa kwani baada ya matibabu kukamilika anaweza kukaa hospitali kwa muda wa masaa machache na kuruhusiwa kurudi nyumbani bila kulazwa wodini”,.

“Faida nyingine inayopatikana katika kambi hii ni  utoaji wa mafunzo ambayo yatawawezesha madaktari kutoka JKCI kuendelea kutoa huduma hizi siku za mbeleni,” alisema Dkt. Kisenge.

Aidha Dkt. Kisenge amewaomba madaktari nchini kutuma wagonjwa waliopo mikoani wenye matatizo ya moyo hasa wenye matatizo ya mishipa ya damu ya moyo iliyoziba ili waweze kupata  matibabu sahihi katika Taasisi hiyo.

Kwa upande wake Daktari mbobezi wa moyo na mzibuaji wa mishipa ya damu ya moyo kutoka Shirika la Madaktari Afrika la nchini Marekani Eric Powers alisema madaktari kutoka shirika hilo wamekuwa wakitoa mafunzo ya mara kwa mara kwa wataalamu  wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete na sasa wanatoa  mafunzo ya uzibuaji wa mishipa ya damu iliyoziba kwa muda mrefu kupitia mishipa iliyopo kwenye mikono.

“Mabadiliko ni makubwa sana katika utoaji wa huduma za matibabu kwa wagonjwa hapa JKCI, mafunzo ya mara kwa mara yameboresha huduma za matibabu na kuwafanya wataalamu wa Taasisi hii kuweza  kumudu kufanya upasuaji wa aina mbalimbali wa magonjwa ya moyo hapa nchini”, alisema Dkt. Powers.

Kambi hiyo inayoenda sambamba na utoaji wa mafunzo kwa wataalamu wa Taasisi hiyo  imedhaminiwa na Kampuni ya Medtronic kwa nchi zilizopo Kusini mwa Jangwa la Sahara ambao ni  watengenezaji  na wasambazaji wa vifaa vinavyotumika katika upasuaji na uzibuaji wa mishipa damu ya  moyo. 
 Wataalamu wabobezi wa moyo na wazibuaji wa mishipa ya damu ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na mwenzao kutoka kampuni ya Medtronic kwa nchi zilizopo Kusini mwa Jangwa la Sahara Dkt. Hani  Abdel  Hadi wakizibua  mishipa ya damu ya moyo ya mgonjwa ambayo imeziba kwa muda mrefu katika kambi maalum ya siku mbili  inayofanyika katika Taasisi hiyo. Kampuni ya Medtronic ni watengenezaji  na wasambazaji wa vifaa vinavyotumika katika upasuaji na uzibuaji wa mishipa ya  moyo wamemtuma mtaalamu huyo katika Taasisi hiyo kwa ajili ya kufundisha na kutoa matibabu yanayohitaji utaalamu wa hali ya juu kwa wagonjwa ambao mishipa yao ya damu ya moyo imeziba.
 Daktari mbobezi wa moyo na mzibuaji wa mishipa ya damu ya moyo kutoka kampuni ya Medtronic kwa nchi zilizopo Kusini mwa Jangwa la Sahara Dkt. Hani  Abdel  Hadi akiwaelekeza wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) namna ya kuzibua  mishipa ya damu ya moyo ambayo imeziba kwa muda mrefu uzibuaji ambao unahitaji utaalamu wa hali ya juu katika kambi maalum ya kufundisha na kufanya matibabu ya siku tatu inayofanyika katika Taasisi hiyo. Jumla ya wagonjwa 12 wanatarajiwa kuzibuliwa mishipa ya damu ya moyo kwa njia ya upasuaji mdogo wa moyo wa bila kufungua kifua kwa kutumia mtambo wa Cathlab (Catheterization Laboratory) ambapo mgonjwa anatobolewa tundu dogo katika mshipa wa damu wa mkono.
Picha na JKCI 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...