Na Said Mwishehe,Michuzi TV
KAMATI Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi(CCM)
imetoa siku saba kwa kamati ndogo ya Udhibiti na Nidhamu inayoongozwa na Makamu Mwenyekiti wa Chama hicho Bara Philip Mangulla kuandaa taarifa ya wanachama watatu ambao ni Abdulrahman Kinana, Yusufu Makamba na Bernard
Membe.
Makamu Mwenyekiti huyo wa CCM kupitia kamati hiyo alipewa jukumu la
kuwahoji wanachama hao kutokana na maagizo ya Halmashauri Kuu ya CCM iliyokutana Desemba mwaka 2019.Hivyo tayari agizo hilo limekamilika kwa
wanachama hao wote kuhojiwa.
Akizungumza leo Februari 12 mwaka 2020 kwa niaba ya Katibu Mkuu wa CCM
Dk.Bashiru Ally, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Chama hicho Humphrey Polepole
amesema pamoja na mambo mengine kikao cha Kamati Maaluum ya Kamati Kuu
ya Halmashauri Kuu Taifa imeielekeza kamati ya mzee Mangulla kuandaa taarifa
ya wanachama hao ambao tayari wamehojiwa.
"Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM imepokea taarifa ya awali ya
kutoka kwa Kamati ya usalama na maadili kuhusu kutekelezwa kwa azimio la
Halmashauri Kuu ya Taifa kuhusu kuwaita na kuwahoji wanachama watatu wa
CCM ambao ni Yusufu Makamba, Abdulrahman Kinana pamoja na Bernard
Membe ambao wote wamekwisha kufika mbele ya Kamati ndogo ya udhibiti na
nidhamu inayoongozwa na Makamu Mwenyekiti wa CCM Philip Mangulla.
"Baada ya kuwasilishwa kwa taarifa hiyo ya awali, Kamati Kuu ya Halmashauri
Kuu imetoa siku saba kwa kamati ndogo ya udhibiti na nidhamu chini ya Mzee
Mangulla kukamilisha taarifa inayohusu wanachama hao watatu na kisha
kuiwasilisha katika kikao husika,"amesema Polepole.
Wakati huo huo Polepole amesema mbali ya kikao cha Kamati Kuu ya
Halmashauri Kuu kupokea taarifa ya kuhojiwa kwa wanachama hao, pia
imepokea maombi ya Waziri Mkuu mstaafu Frederick Sumaye ya kuomba
kujiunga na CCM.Kamati Kuu imeridhia na imempongeza Sumaye na kutaka
kufuatwa kwa taratibu za kujiunga na Chama hicho.
Polepole amesema Kamati Kuu imepokea taarifa ya maandalizi ya muelekeo wa
sera za CCM kwa mwaka 2020/2030 na uandishi wa Ilani ya CCM ya Uchaguzi
Mkuu kwa mwaka 2020 ambayo itakuwa ya mwaka 2020/2025.Pia Kamati Kuu
imepokea waraka wa uandishi huo na kujiridhisha na kazi nzuri ambayo
imefanyika mpaka hapo ilipofikia.
"Kikao cha Kamati Kuu pia kimepongeza kazi nzuri ambayo inafanywa na Chama
na Serikali katika kutekeleza Ilani na hivyo kuleta heshima kubwa kwa Chama
chetu,"amesema Polepole.
Mwisho
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...