Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Anamringi Macha akielezea mafanikio ya Soko la Madini la Kahama na vituo vya ununuzi wa madini kwa wanahabari kutoka Idara ya Habari MAELEZO (hawapo pichani) tarehe 06 Februari, 2020.
Mchambuzi wa Madini ya Almasi wa Tume ya Madini Nelson Magawa, akithaminisha baadhi ya madini ya almasi katika Soko la Kimataifa la Madini ya Almasi na Dhahabu lililopo mjini Shinyanga.
Mfanyabiashara kutoka kampuni ya Fretja Natural Energy Resources Tanzania Ltd, Teddy Goliama (kulia) akipima madini ya almasi ya mteja katika Soko la Kimataifa la Madini ya Almasi na Dhahabu lililopo mjini Shinyanga.
*******************************
Wadau mbalimbali wa madini pamoja na viongozi waandamizi katika mkoa wa Shinyanga wamempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Magufuli, Wizara ya Madini pamoja na Tume ya Madini kwa hatua ya uanzishwaji na usimamizi wa masoko ya madini na vituo vya ununuzi wa madini kwani yameleta mabadiliko ya kiuchumi katika mkoa wa Shinyanga.
Wakizungumza na timu ya maafisa habari kutoka Idara ya Habari MAELEZO na Tume ya Madini kwenye ziara ya maandalizi ya vipindi vinavyohusu mafanikio ya masoko ya madini katika mkoa wa Shinyanga leo tarehe 06 Februari, 2020 mbali na kupongeza juhudi zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano, wameeleza kuwa masoko ya madini yameleta mapinduzi makubwa ya kiuchumi ikiwa ni pamoja na ajira, mapato kwa Serikali na kuongeza kasi ya ukuaji wa shughuli za uchimbaji wa madini katika mkoa huo.
Akizungumza ofisini kwake Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Anamringi Macha alisema kuwa, kabla ya kuanza kwa masoko ya madini katika Mkoa wa Kimadini wa Kahama, Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Shinyanga ilikuwa inakusanya jumla ya kiasi cha shilingi milioni 593.6 kwa mwaka, lakini baada ya masoko kuanzishwa mapema Julai mwaka jana hadi kufikia Januari, 2020 ofisi hiyo imeweza kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 9.7.
Macha alieleza mafanikio mengine kuwa ni pamoja na kuongezeka kwa udhibiti wa utoroshwaji wa madini hali iliyopelekea uzalishaji wa madini katika Mkoa wa Kimadini wa Kahama kuongezeka kutoka kilo 100 kwa mwaka hadi kilo 1572 tangu kuanzishwa kwa masoko ya madini.
Aliongeza kuwa elimu ya uzalendo imekuwa ikitolewa mara kwa mara kwa wachimbaji na wafanyabiashara wa madini ambapo katika Wilaya ya Kahama kila mchimbaji anapopata madini hupeleka katika Soko la Madini la Kahama na vituo vya ununuzi wa madini na kupata faida kubwa pasipo kudhulumiwa.
Katika hatua nyingine, Macha aliwataka masonara kupokea madini kutoka kwenye masoko ya madini yaliyoanzishwa badala ya kununua moja kwa moja kwa wachimbaji na kuongeza kuwa kutotumia masoko ya madini yaliyoanzishwa ni kinyume na sheria.
Aidha, mbali na kumpongeza Rais Magufuli, Waziri wa Madini, Doto Biteko na Tume ya Madini kwa ujumla, Macha alitumia fursa hiyo kupongeza vyombo vya ulinzi na usalama ambavyo vimekuwa vikifanya kazi usiku na mchana katika udhibiti wa utoroshwaji wa madini nchini.
Pia, aliwataka wawekezaji wanaopewa leseni za utafiti wa madini kuanza shughuli za utafutaji wa madini badala ya kuacha maeneo kukaa wazi kwa muda mrefu hali inayopelekea kuvamiwa na kuleta migogoro.
Naye mfanyabiashara mdogo wa madini aina ya almasi katika Soko la Kimataifa la Madini ya Almasi na Dhahabu lililopo mjini Shinyanga, Jafari Kashinde alisema kuwa soko hilo limeleta mabadiliko makubwa kwenye biashara ya madini ya almasi katika mkoa wa Shinyanga kwa kuwa kabla ya kuanzishwa kwa soko hilo biashara ilikuwa ikifanyika kwa kificho na madini kutopatikana kwa urahisi.
Alieleza manufaa mengine ya soko hilo kuwa ni pamoja na kufanyiwa uthaminishaji wa madini hayo na wataalam kutoka Tume ya Madini hivyo kuepushwa na utapeli na wafanyabiashara wasio waaminifu.
Naye mfanyabiashara wa madini kutoka kampuni ya Tripple A Diamond Group Co ltd, Ali Ahmed aliongeza kuwa manufaa mengine katika soko hilo ni pamoja ulinzi ulioimarishwa na mazingira mazuri ya ulipaji kodi yaliyowekwa na Tume ya Madini.
Aidha, mfanyabiashara mwingine wa kutoka kampuni ya Fretja Natural Energy Resources Tanzania Ltd, Teddy Goliama mbali na kuipongeza Serikali kwa uanzishwaji wa soko hilo, aliongeza kuwa heshima kwa nchi kwenye umiliki wa uchumi wa madini imeongezeka kwa kuwa awali madini yalikuwa yakitoroshwa nje ya nchi na wafanyabiashara wasio waaminifu hivyo kudhaniwa yanapatikana nchi nyingine.
“Mfano hai ni madini ya Tanzanite ambayo yanapatikana Tanzania pekee, kabla ilikuwa inafahamika yanapatikana pia katika nchi nyingine kutokana na kutoroshwa kwa wingi lakini baada ya ujenzi wa ukuta wa Mirerani na uanzishwaji wa masoko ya madini, sasa inafahamika kuwa madini ya Tanzanite yanapatikana Tanzania pekee,” alisisitiza Goliama.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Shinyanga Vijijini, Hoja Mahiba alisema kuwa, mara baada ya kuweka utaratibu mzuri wa usimamizi wa uchimbaji wa madini katika eneo la wachimbaji wadogo wa madini la Mwakitolyo eneo hilo limeanza kuzalisha gramu 300 hadi gramu 500 kwa siku tofauti na awali ambapo kulikuwa hakuna kinachopatikana.
Aliongeza kuwa mafanikio mengine kuwa ni pamoja na halmashauri ya Shinyanga Vijijini kukusanya kiasi cha shilingi milioni 77 kwa nusu mwaka wa fedha 2019/2020 tofauti na mwaka 2018/2019 ambapo walikusanya shilingi milioni 73 tu.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...