Tanzania imeieleza Tume
ya haki za binadamu na watu wa Afrika ya Umoja wa Afrika kuwa kuna
tofauti kati ya makosa ya kitaalamu na makosa ya jinai na kwamba Sheria
inapochukua mkondo wake isitafsirike kuwa ni kukiuka haki za binadamu
kwa kuwa Nchini Tanzania hakuna raia wake yeyote aliye juu ya sheria
pale anapotenda kosa la jinai.
Waziri
wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba
John Kabudi ameyasema hayo katika majadiliano ya taarifa ya Tume ya Haki
za Binadamu katika mkutano wa 33 wa Baraza la Mawaziri wa Umoja wa
Afrika unaofanyika Addis Ababa Nchini Ethiopia na kuongeza kuwa Tanzania
inaheshimu haki za binadamu,uhuru wa kujieleza na uhuru wa vyombo vya
habari kama ilivyo katika katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Prof.
Kabudi ameongeza kuwa Nchini Tanzania hakuna raia wake aliye juu ya
sheria na kwamba pale mwanataaluma anapofanya makosa ya kijinai
huchukuliwa hatua za kisheria kama ilivyo kwa wananchi wengine kwa
kufikishwa katika vyombo rasmi vya kutoa haki kama mahakama ambayo iko
huru kufanya maamuzi yake isichukuliwe kama ukiukwaji wa haki za
binadamu au kuminya uhuru wa kujieleza.
Amesema
kuwa kuna baadhi ya wananchi wa Tanzania ambao wamekuwa wakitumia
taaluma zao vibaya na hivyo kuwafanya kutenda makosa ya jinai kwa
kutumia taaluma zao na hivyo kufikishwa mbele ya sheria na kuongeza kuwa
mashauri yao yako mahakamani na vyombo vingine vya sheria na ana imani
mahakama na vyombo hivyo vitatoa haki dhidi ya mashtaka yanayowakabili
baada ya kutoa utetezi wao mbele ya vyombo hivyo.
Hivi
karibuni kumekuwepo na mjadala kutoka kwa baadhi ya
wanaharakati,wanasiasa na Jumuiya za Kimataifa zikiishutuma Tanzania
kukiuka haki za binadamu jambo ambalo serikali imeiambia Umoja wa Afrika
na Jumuiya za Kimataifa kuwa si kweli na kwamba Tanzania inaheshimu
haki za binadamu na uhuru wa kujieleza.
Mkutano
wa kawaida wa 33 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika
unafanyika Mjini Addis Ababa Nchini Ethiopia ukitanguliwa na mikutano
mbalimbali ya Baraza la Mawaziri na baadae Wakuu wa Nchi na Serikali na
unatarajiwa kumalizika Februari 10,2020.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...