Mkataba wa Utekelezaji wa Miradi ya Maendeleo ya Wananchi ndani ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro, umesainiwa rasmi leo tarehe 26 mwezi Machi 2020 jijini Dodoma kati ya Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro , Baraza la Wafugaji la wananchi wa Ngorongoro na Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro,

Mkataba huo unafuatia agizo la Serikali la kuitaka Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kuhamisha fedha zote zilizokuwa zinalipwa kwa Baraza la Wafugaji la wananchi wa Ngorongoro kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwenda Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro.

Baada ya mkataba huo kusainiwa mbele ya Waziri wa Maliasili na Utalii, sasa Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro ndiyo itakuwa mtekelezaji wa miradi ya maendeleo ndani ya Tarafa ya Ngorongoro na baraza la Wafugaji watakuwa wafuatiliaji wa utekelezaji wa miradi hiyo.

Ufuatiliaji huo pia utafanywa na Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro.

Katika mkataba huo, kuna timu ya wataalam inayojumuisha wajumbe sita kutoka pande zote husika ( Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro, Baraza la Wafugaji Eneo la Ngorongoro na Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro).

Kamati hiyo itaongozwa na Mwenyekiti ambaye ni Meneja wa Maendeleo ya Jamii kutoka Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro na itahusisha wajumbe wengine Watano, ambapo wajumbe wawili watatoka kwenye Baraza la Wafugaji Eneo la Ngorongoro , wawili kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro na mmoja kutoka Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro.

Kuridhiwa na kusainiwa kwa Mkataba huo, kunatarajiwa kuwezesha utekelezaji mzuri wa miradi ya maendeleo kwa wananchi wanaoishi katika Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro.

Kusainiwa kwa Mkataba huo kumeshuhudiwa na Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dkt. Hamisi Kigwangalla ( Mb.) aliyekuwa Mwenyekiti wa mkutano huo, Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi, na Teknolojia Mhe. William Ole Nasha, Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Prof. Adolf Mkenda, Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro Dkt. Rashid Mfaume Taka, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro Mhe. Mathew Siloma na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro Prof. Abiud Kaswamila.

Wengine walioshuhudia kusainiwa kwa mkataba huo ni, Mwakilishi wa Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro, Bw. Abdalah Kiwango, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro, Bw. Raphael Siumbu na Mwenyekiti wa Baraza la Wafugaji Eneo la Ngorongoro, Mhe. Maura Ole Ndule. Waziri wa Maliasili na Utaliii, Dkt. Hamisi Kigwangalla akizungumza wakati wa mkutano na viongozi wa Wilaya ya Ngorongoro, Viongozi wa Baraza la Wafugaji Ngorongoro na Uongozi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro kuhusu utaratibu wa usimamizi wa fedha zinazotolewa na Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro kwa ajili ya Baraza la Wafugajji na miradi inayotekelezwa katika Tarafa ya Ngorongoro . Kushoto kwa Waziri Kigwalla ni Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii Prof. Adolf Mkenda, na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro Prof. Abiud Kaswamila.
Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro, Bw. Rashid Mfaume Taka, (kushoto) akizungumza na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro, Prof. Abiud Kaswamila mara tu baada ya kumaliza mkutano wa kujadili utaratibu wa usimamizi wa fedha zinazotolewa na Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro kwa ajili ya Baraza la Wafugajji na miradi inayotekelezwa katika Tarafa ya Ngorongoro .

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...