KADCO yajenga chumba cha barafu chenye uwezo wa kubeba tani 110
Na Prisca Ulomi, WUUM, KIA
Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye amezindua safari za ndege za mizigo kwenye Uwanja wa Ndege wa Kilimanjaro (KIA) kwa ajili ya kuwawezesha wafanyabiashara, wakulima wa mazao, matunda na mboga mboga wa mikoa ya Kilimanjaro, Arusha, Tanga, Manyara na mikoa ya jirani kutumia usafiri huo kusafirisha mizigo yao kwenda nje ya nchi ya Tanzania
Nditiye amesema kuwa uzinduzi wa safari za ndege za mizigo ni utekelezaji wa agizo la Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isack Kamwelwe wakati akizindua bodi ya Maendeleo ya Kiwanja cha Ndege cha Kilimanjaro (KADCO) mwaka jana mwezi Desemba
“Niwapongeze sana KADCO kupitia Kaimu Mkurugenzi Mkuu wenu, Christopher Mukomu na kwa kushirikiana na Umoja wa Wakulima wa Mboga Mboga na Maua Tanzania (TAHA), mmeweza na kuhakikisha ujio wa ndege hii muhimu kwa ajili ya kusomba mizigo yetu hapa Tanzania, hilo kwangu mimi ni kitu kikubwa sana kwa sababu kwa miaka mingi hatukuwa na huduma ya mizigo kwa ndege kubwa kama hii, naipongeza sana Ethiopian Airline kwa utayari wao wa kushirikiana na Serikali na kuamua kuleta ndege yao ya mizigo kuja kubeba mizigo,” amesema Nditiye
Pia, amekagua chumba cha barafu cha kuhifadhi mizigo inayosafirishwa na ndege kwenda nje ya nchi ya Tanzania na kujiridhisha kuwa chumba hicho cha kisasa kimejengwa, kinafanya kazi vizuri na kina uwezo wa kubeba tani 110 na kina hali nzuri na amewaomba wadau mbali mbali kutumia huduma hii kusafirisha mizigo yao badala ya kupitisha nchi za jirani
Ameilekeza Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) kukaa na wadau wa usafirishaji wa mizigo hiyo ili kuweza kutoa kibali cha muda mrefu cha wiki mbili au hata mwezi ili kuwawezesha wasafirishaji kutumia vizuri fursa hii na amewataka wazingatie sheria, taratibu na kanuni husika na siyo kutoa kibali tu, bali kutoa kibali cha kuhakikisha kuwa biashara hii inakuwa endelevu na kuzingatia usalama
Nditiye ametoa maelekezo hayo baada ya Afisa Mtendaji Mkuu wa TAHA, Dkt. Jacquline Mkindi kuiomba Serikali kuweka mazingira wezeshi ya usafirishaji wa mizigo kwenda masoko ya Ulaya ikiwa ni pamoja na ndege hizo kuja nchini kwa gharama nafuu kwa kupunguza tozo mbali mbali kwa ndege kila inapotua, kuongeza muda wa kibali cha ndege na kuwa na tozo tofauti baina ya ndege za mizigo na za abiria ili kuendelea kuzivutia ndege hizo na ndege nyingine za mizigo kuja KIA na kutumia fursa hiyo kuiwezesha sekta binafsi na wakulima wa mboga mboga na maua kufanya biashara kwenye soko lolote duniani
Uzinduzi wa safari za ndege za mizigo umehudhuriwa na Waziri wa Kilimo, Japhet Hasunga ambapo ameshuhudia wakulima wa mboga mboga na maua wa TAHA wakipakia mizigo ya bidhaa zao kwenda nje ya nchi ambapo Nditiye na Hasunga wameshiriki kupakia mizigo hiyo
Naye Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Anna Mghwira amesema kuwa Serikali inatambua mchango wa sekta binafsi na wakulima na lazima sekta binafsi ikuzwe a ilelewe kwa kupewa mashaerti nafuu ya kufanya biashara zao na itaendelea kuunganisha mnyororo wa thamani kwa kutumia viwanja vyake vya ndege na kununua ndege za mizigo kama ambavyo Serikali imefanya kwa kununua ndege za abiria
Nditiye amefafanua kuwa kwa muda mrefu ndege ya KLM imekuwa ikitumia uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere uliopo Dar es Salaam kusafirisha mizigo kwenda nchi mbali mbali, Serikali imeanza kujenga chumba cha barafu cha kuhifadhi mizigo kwenye uwanja wa ndege wa Mbeya na katik mwaka wa fedha wa 2020/2021, Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano imetenga fedha ya kununua ndege ya kusafirisha mizigo
Naibu Waziri wa
Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye akizungumza na waandishi wa
habari baada ya kuzindua safari za ndege za mizigo kwenda nje ya nchi ya
Tanzania kwenye Uwanja wa Ndege wa Kilimanjaro
Naibu Waziri wa
Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye akitoka ndani ya ndege baada
ya kuzindua safari za ndege za mizigo kwenda nje ya Tanzania kwenye uwanja wa
Ndege wa Kilimanjaro. Anayemfuata ni Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa KADCO,
Christopher Mukomu
Naibu Waziri wa
Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye (wa pili kulia) akishirikiana
na wafanyakazi kupanga mizigo baada ya kuzindua ndege ya kusafirisha mizigo
kwenda nje ya nchi kwenye Kiwanja cha Ndege cha Kilimanjaro
Naibu Waziri wa
Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye (wa kwanza kushoto)
akijadiliana na Waziri wa Kilimo, Japhet Hasunga (wa kwanza kulia) mara baada
ya kuzindua safari safari za ndege za mizigo kwenda nje ya nchi kwenye Uwanja
wa Ndege wa Kilimanjaro
Naibu Waziri wa
Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye akitoa maelekezo kwa Kaimu
Mkurugenzi Mkuu wa KADCO, Christopher Mukomu (wa pili kulia) wakati akikagua chumba
cha barafu cha kuhifadhia mizigo kilichopo kwenye Uwanja wa Ndege wa
Kilimanjaro
Mkuu wa Mkoa wa
Kilimanjaro, Anna Mghwira (kushoto) akizungumza na Naibu Waziri wa Uchukuzi na
Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye (wa pili kulia) wakati wakisubiri
kuwasili kwa ndege ya mizigo kutoka nje ya nchi kwenye Uwanja wa Ndege wa
Kilimanjaro
Meneja Biashara na
Masoko wa KADCO, Christine Mwakatobe (wa tatu kushoto) akifafanua jambo kwa
Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye kabla ya
kuzindua safari za ndege za mizigo kwenye Uwanja wa Ndege wa Kilimanjaro
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...