Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Bw.
Gerald Kusaya akitazama majani makavu ya chai yaliyotayari kupelekwa
sokoni wakati alipokagua kiwanda cha chai Wakulima (WATCO ) Tukuyu.
Mkurugenzi Mkuu wa kampuni ya Chai
Wakulima Bw. Andres de Klerk (kushoto) akikabidhi zawadi ya majani ya
chai kwa Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Bw. Gerald Kusaya mara baada ya
kutembelea kiwanda hicho Tukuyu wilayani Rungwe
Katibu
Mkuu Wizara ya Kilimo Bw. Gerald Kusaya (kushoto) akikabidhi mashine ya
kisasa ya kuvunia majani mabichi ya chai kwa mkulima. Mashine hizo
zimenunuliwa na Chama cha Ushirika wa Wakulima Wadogo wa Chai wa Rungwe
na Busokelo (RUBUTCO-JE)
( Habari na Picha na Wizara ya Kilimo)
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Bw.
Gerald Kusaya ( suti ya blu) akiwa na mwakilishi wa kampuni ya METL Bw.
George Mwamakula (kushoto) wakati akikagua kiwanda cha chai Chivanjee
Tukuyu Rungwe leo.Kiwando hicho hicho hakifanyi kazi tangu Aprili mwaka
huu na kusababisha kero kwa wakulima.
Kiwanda cha chai Chivanjee
kilichopo katika shamba la chai Tukuyu kikiwa kimefungwa bila kufanya
kazi. Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Gerald Kusaya ameagiza uongozi wa
METL kujieleza kwanini umesitisha uzalishaji na ununuzi wa chai ya
wakulima kinyume na makubaliano.
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo
Gerald Kusaya (kulia) akiwa kwenye mazungumzo na Mkuu wa Wilaya ya
Rungwe Mhe. Chalya Nyangindu (kushoto) kuhusu maendeleo ya zao la chai
wakati wa ziara yake kutembelea wadau wa zao hilo.
……………………………………………………………………………………..
Serikali imeagiza kampuni ya
Mohamed Enteprises (METL) inayomiliki shamba la chai la Tukuyu kutoa
maelezo kuhusu matumizi ya shamba hilo ni kwa namna gani wameweza
kuliendeleza tangu walipokabidhiwa mwaka 2007 ikiwemo viwanda vya chai.
Akizungumza na uongozi wa kampuni
METL leo (15.07.2020) wakati alipotembelea kiwanda cha chai Chivanjee
kilichopo Tukuyu, Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Gerald Kusaya alisema
hajaridhishwa na sababu za kufungwa kwa viwanda vya chai.
Katibu Mkuu huyo alifanya ziara
katika shamba la chai Tukuyu ( Tukuyu Tea Estate) na kujionea kiwanda
kikiwa kimesitisha ununuzi wa majani mabichi ya chai na uchakataji toka
mwezi Aprili mwaka huu hali inayoathiri wakulima wa Rungwe.
“ Binafsi kama Katibu Mkuu bado
sijashawishika kama kampuni ya METL ina jitihada za makusudi za kufungua
viwanda hivi vya Chivanjee na Musekera ili wakulima wa chai wapate
soko na nchi ipate mapato yake ” alisema Kusaya.
Kufuatia hali hiyo ,Katibu Mkuu
huyo alitoa maagizo mawili kwa wamiliki wa viwanda hivyo kuwa kabla ya
tarehe 30 Julai mwaka huu wawasilishe ofisini kwake Dodoma taarifa ya
kina inayo onyesha ukubwa wa eneo, kiasi kilichopandwa chai na ipi
mikakati ya kampuni kuendeleza ardhi waliopewa na serikali.
“Katika taarifa hiyo nataka METL
muwe wakweli kabla ya kuileta kwangu ili tujirishishe na ukubwa wa
shamba hili na matumizi yake” alisisitiza Kusaya.
Kusaya alitaja agizo la pili kuwa
METL iwasilishe taarifa kwa Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara
kabla ya tarehe 30 Julai mwaka huu kuelezea mikakati na mpango kazi wa
kufufua viwanda vyote viwili.
Katibu Mkuu huyo aliongeza kusema
endapo kampuni METL itapeleka taarifa isiyoshawishi serikali, wizara ya
Kilimo kwa kushirikiana na Wizara ya Viwanda na Biashara na ile ya Ardhi
watamshauri Rais achukue hatua za kuyatwaa mashamba hayo kwa manufaa ya
umma.
“ Kama mtaleta taarifa isiyo na
ushawishi kwa serikali, nitaongea na wenzangu wa Viwanda na Ardhi kwenda
kumuomba Rais Dkt. John Pombe Magufuli ili ayatwae mashamba na viwanda
vilivyopewa METL kwa mujibu wa sheria ili apatiwe mtu mwingine mwenye
uwezo wa kuyaendeleza ” alisema Kusaya.
Kwa upande wake Mwakilishi wa
kampuni ya METL George Mwamakula alisema sababu iliyopeleka kiwanda cha
Chivanjee kusitisha ununuzi wa chai zilitokana na watu waovu kuiba
mashine pamoja na miundombinu ya umeme, mota, vyuma na mfumo wa maji.
Kuhusu kiwanda cha Musekera
kufungwa kampuni ya METL ilisema imepanga kianze kazi mwaka 2022 baada
ya ufungaji mitambo mipya na kukarabati miundombinu.
Katika hatua nyingine Katibu Mkuu
Kusaya alitembelea Chama cha Ushirika wa Kilimo na Masoko (ROTCO) cha
Tukuyu na kuwasihi waache kugomea kuuza chai yao kwenye kampuni tanzua
ya Wakulima Tea Company (WATCO) .
Mgogoro wa ushirika wa wakulima wa
chai Rungwe umepelekea wanachama wa ROTCO kutotaka kwenda kuuza majani
mabichi kwenye kiwanda cha WATCU wakidai kuwa hawatambui umoja huo na
kutaka serikali iwazuie kufanya kazi hadi utatuzi wa mgogoro
utakapoisha.
Katibu wa ushirika wa ROTCO Amos
Mwakasengo aliomba serikali iagize kampuni ya Mohamed Enteprises
kutekeleza mkaba wa mauzo ya chai na ushirika huo kufuatia kusitisha
ununuzi wa majani ya chai bila taarifa kunakoathiri wakulima.
Kusaya alitoa wito kwa wanachama
wa ROTCO wakati majadiliano ya kutafuta suluhu yakiendelea wapeleke
majani mabichi ya chai kiwanda cha WATCU kuuza na kujipatia kipato
badala ya kuacha ikiharibika shambani.
Aidha Kusaya alitembelea Ushirika
wa Wakulima Wadogo wa Chai Rungwe na Busokelo ( RUBUTCO-JE) ambapo
amewata wakutane na Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB) kuona namna
watakavyoweza kupata mtaji wa kuanzisha kiwanda cha chai cha ushirika
huo ili kuwa na uhakika wa soko la chai .
Katibu Mkuu huyo wa Wizara ya
Kilimo alitembelea pia kiwanda cha parachichi Rungwe (RAC) na kukitaka
kisitishe uamuzi wake wa kutonunua parachichi za wakulima kwa kigezo cha
kukosa ubora.
Mwisho
Imetolewa na;
Kitengo cha Mawasiliano Serikalini
Wizara ya Kilimo
TUKUYU,MBEYA
15.07.2020
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...