Katibu Tawala wa Wilaya ya Kondoa akitoa rai kwa wananchi wa Kondoa kuitumia Mahakama ili kusuluhisha migogoro yao.
Hakimu Mkazi Mfawidhi Mwandamizi wa Mahakama ya Wilaya Kondoa akitoa ufafanuzi juu ya maboresho ya miundombinu ya Mahakama yalivyorahisisha utoaji haki kwa wakati.Jengo Jipya la Mahakama ya Wilaya ya Kondoa linalotumika kutoa huduma za kimahakama.Picha na MAHAKAMA na Idara ya Habari-MAELEZO 
**********************************
Na Innocent Kansha – Mahakama Kondoa
Mahakama ya wilaya ya Kondoa imesikiliza na kumaliza mashauri ya jinai na madai 184 kati ya mashauri 262 yaliyokuwepo katika Mahakama za wilaya za Kondoa na Chemba.

Akizungumza na Maafisa Habari wa Mahakama ya Tanzania, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mwandamizi wa Mahakama ya Wilaya ya Kondoa Mhe. Francis Robert Mhina alisema mashauri hayo yamesikilizwa na kumalizika kati ya mwezi Januari na Julai, mwaka huu.

“Mashauri yaliyobaki mwezi Desemba 2019 yalikuwa ni 152, yaliyosajiliwa kati ya Januari na Julai mwaka huu ni mashauri 110, tumesikiliza na kumaliza jumla ya mashauri 184 na kubakiwa na mashauri 78”, alifafanua Mhe. Mhina.

Kwa mujibu wa Hakimu Mfawidhi huyo, asilimia kubwa ya mashauri yanayofunguliwa kwenye Mahakama hizo ni yale yanayohusu ukatili wa kijinsia ikiwemo ubakaji, pamoja na mauaji, kujeruhi na mashauri ya kukutwa na nyara za wanyama pori.Alisema mashauri yanayohusu nyara za taifa hasa wanyama pori yanatokana na uwepo wa mapori tengefu ya hifadhi za Swaga swaga na Mkungunero.

“Wananchi wengi wanaoishi kando kando ya hifadhi hizi wamekuwa wakiendesha shughuli zao mbalimbali za kiuchumi bila kuzingatia mipaka na kujikuta wanakinzana na sheria za hifadhi kama kulima ndani ya hifadhi, kuvua samaki, kuchoma mkaa, kukutwa na nyara za Taifa na kuwinda wanyama pasipo kuwa na vibali halali”, alisema Mhe. Mhina.
Mhe. Mhina alisema asilimia kubwa ya mashauri ya mauaji yanatokea Wilaya ya Chemba. Mahakama ya Wilaya ya Kondoa pia inahudumia Wilaya Chemba kwa sasa.

Kuhusu matumizi ya Tehama katika Mahakama ya wilaya ya Kondoa, Mhe. Mhina amesema yamesaidia kwa kikubwa kurahisisha suala la upatikanaji wa haki kwa wakati. Aliongeza kuwa mfumo wa kusajili mashauri (JSDS II) unatumiwa vizuri na watumishi katika kutunza kumbukumbu za kila siku za mashauri baada ya kufungiwa mkongo wa Taifa wa mawasiliano.

Naye Katibu Tawala wa Wilaya ya Kondoa Bw. Andrea Ng’hwani alisema Serikali Wilayani humo imeyapokea maboresho ya miundombinu ya Mahakama kwa furaha kwani yametatua changamoto na kero za wananchi wa Kondoa kwa kiasi kikubwa.

“Nawakumbusha wananchi kuwa nchi hii inaongozwa kwa misingi ya kisheria na hakuna mazingira yoyote yanayoruhusu mtu kujichukulia sheria mikononi ndiyo maana kuna Jeshi la Polisi na Mahakama ili kutatua kero zao” alisisitiza Katibu Tawala.

“Kero za wananchi zimepungua sana na sasa hatupokei malalamiko yanayohusu Mahakama kiutendanji na mambo mengine yanayohusu uelewa wa taratibu za kimahakama tumekuwa mstari wa mbele kuyatolea ufafanuzi wa kuwaelekeza sehemu sahihi ya kutatua na kupata ufafanuzi”, alisema Katibu Tawala. 
Bw. Ng’hwani alisema wananchi wanapaswa kupeleka migogoro yao mahakamani ili iweze kutatuliwa kisheria na pale wanapoona hawajaridhika na maamuzi, wakate  rufaa Mahakama ya juu zaidi kupata haki ili Amani na utulivu vizidi kuimarika.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...