Mtaalamu wa Afya kutoka Shirika la Save The Children Victor Minja, akizungumza wakati wa ufunguzi wa warsha hiyo iliyolenga kupata suluhu za athari ziletazwo na majanga kama Covid-19, ambapo ameeleza kuwa Shirika hilo litaendelea kushirikiana na Serikali katika kusongesha mbele gurudumu la maendeleo ya Jamii na taifa,leo jijini Dar es Salaam.
Meneja wa Uchechemuzi na Kampeni kutoka Save The Children, Nuria Mshare akizungumza na wanahabari wakati wa ufunguzi wa warsha hiyo na kusema kuwa Shirika hilo linaamini suluhu za Athari ziletazwo na majanga kama Covid-19 hutoka kw makundi husika, leo jijini Dar es Salaam.


Akizungumza na wanahabari mara baada ya warsha hiyo mtaalamu wa Afya kutoka save the Children Victor Minja, ambaye pia alimwakilisha Mkurugenzi wa Save The Children amesema kuwa, Shirika hilo lisilo la kiserikali limekuwa likishirikiana kwa ukaribu zaidi na Serikali wakati wa majanga mbalimbali katika kuhakikisha jamii inabaki salama wakati wa majanga na baada ya hapo.
Amesema, katika warsha hiyo wametoka na ajenda ambazo zikitiliwa mkazo jamii itakua salama zaidi.
"Kati ya ajenda ambazo tumetoka nazo ni pamoja na Serikali, jumuiya za kimataifa, taasisi za kifedha na binafsi kuwalinda watoto na wanawake ambao wapo hatarini zaidi dhidi ya vitendo vya unyanyasaji ukiwemo wa kingono, unyanyasaji majumbani na ndoa za utotoni wakati na kabla ya majanga....makundi haya lazima yapewe kipaumbele katika mikakati na mipango ya Serikali pindi inapokabiliana na majanga mbalimbali ikiwemo Covid-19" ameeleza.
Pia ajenda nyingine ambazo kupitia warsha hiyo zilipendekezwa kutiliwa mkazo zaidi na Serikali,umoja wa mataifa, jumuiya za kimataifa, taasisi za kifedha na sekta binafsi ni pamoja na kuhakikisha makundi maalumu yanakuwa na sauti zinazosikika kwa kuwashirikisha katika sera, mikakati na utekelezaji wa mipango ya kujikwamua katika majanga ili kusaidia jamii kuona hali zao zinajaliwa na sauti zao zinafanyiwa kazi.
Aidha imependekezwa kuwa fedha zaidi ziongezwe kwa nchi masikini ili jamii za hali duni na walio pembezoni waweze kupata haki na mahitaji yao ya msingi wakati wa majanga na baada ya majanga na hiyo ni pamoja na kuzuia familia zisiangukie katika dimbwi la umaskini uliopitiliza kwa kuwasogezea huduma muhimu za kijamii ikiwemo afya, chakula, elimu na malazi.
Kwa upande wake Meneja wa Uchechemuzi na Kampeni kutoka Save The Children Nuria Mshare amesema; Shirika hilo limekuwa likizingatia ushiriki na ushirikishwaji wa makundi maalumu, na kupitia warsha hiyo ambayo imewakutanisha watoto, wanawake na watu wenye ulemavu ni sehemu ya kusikia sauti kutoka kwao juu ya changamoto wakati wa majanga na baada ya majanga na kupata suluhu za changamoto zinazotokana na majanga hao.
"Save The Children tunaamini suluhu zinatoka kwa makundi husika ambayo yanakumbwa na changamoto wakati wa majanga kama janga la Covid-19 lilivyotuonesha.... na hivyo tunaomba jamii, wananchi, serikali na jumuiya za kimataifa kuwalinda watoto, wanawake na watu wenye ulemavu dhidi ya unyanyasaji wa aina yoyote wakati na baada ya majanga na hiyo ni pamoja na kushirikisha sauti zao katika mikakati mbalimbali' amesema.
Shirika lisilo la Serikali la Save The Children limekuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha haki na usawa kwa jamii unazingatiwa na hiyo ni pamoja na kushirikiana na Serikali katika kutatua changamoto katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu na afya kwa kuhusisha makundi maalumu hasa watoto, wanawake na watu wenye ulemavu.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...