*Awaomba wananchi kuichagua CCM washuhudie maendeleo

Na Said Mwishehe, Michuzi TV-Karatu

MGOMBEA urais kupitia Chama Cha Mapinduzi(CCM) Dk.John Magufuli amewataka wananchi wa Wilaya ya Karatu mkoani Arusha kuhakikisha katika uchaguzi Mkuu mwaka huu wanamchagua kwa kura nyingi yeye kwa nafasi ya Rais na pamoja na mgombea ubunge wa jimbo hilo Daniel Awack ili washirikiane kuleta maendeleo.

Dk.Magufuli amesema katika kipindi cha miaka mitano Karatu imekuwa chini ya upinzani na kusababisha maendeleo kuchelewa kupatikana, hivyo amewaomba wananchi hao kuchagua Awack huku akisisitiza kama wamekuwa upinzani kwa muda wote huo waipe CCM hata kwa miaka mitano tu ili waone maendeleo yatakayofanyika.

Akizungumza mbele ya maelfu ya wananchi leo Oktoba 24, 2020, Dk.Magufuli amesema amefika Karatu kuomba kuomba kura zake kwa nafasi ya Rais, kumuombea kura mgombea ubunge pamoja na madiwani.

"Kama mmekaa kule miaka 25 naomba mje na huku CCM,  tuna mgombea wetu , alikuwa mjumbe wa NEC, mkulima mwenzenu, analima vituu.Wanasema hana digrii , ninyi watu wote hapa mna digrii, wanasema hana digrii, huyu ndio ninayemtaka, namtaka Daniel, mnahitaji Mbunge anayeyetea watu, mbunge atakeyesemea shida za watu, nahitaji mbunge atakeyekuwa kiunganisho kati ya wananchi na Serikali.

"Karatu nileteeni Daniel , nawaomba vyama vyote na wasio na vyama tuache tofauti, tunahitaji maendeleo kuliko Chama, kueleza shida za watu unahitaji digrii?Kueleza uhitaji wa barabara ya Mburu hadi Karatu unahitaji digrii?CCM ni Chama cha wakulima,wafugaji na wavuvi, mtu kuwa mbunge sio lazima uwe na digrii.Tunao wachungaji, masheikh, maaskofu wasiokuwa na digrii lakini wanatongoza vizuri,  tuna wazazi wetu hawana digrii lakini wanatunza vizuri watoto wao.

"Nina muhitaji Daniel ambaye hana digrii, mkinifanyia hilo, hamtajuta na ninawapenda sana, Karatu iko katika moyo wangu, ninaipenda, nisingechagua mtu wa Karatu Dk.Wilbrod Slaa kuwa Balozi kuniwakilisha katika nchi tisa.Daniel hajui kujieleza hana maneno mengi, unakuwa na maneno mengi kwani unataka kuoa? Huyu ni mtu wa vitendo,"amesema Dk.Magufuli.

Amesema anamfahamu Awack kwa undani kwa kutumia vyombo vyake, Karatu kama wanataka maendeleo wampelekee Daniel."Nafagamu kero za Karatu, nafahamu maombi yenu ya kituo cha afya Karatu Mjini kwasasababu hapa watu  ni wengi, nileteeni Daniel, mnahitaji kujengewa hospitali ya Wilaya, kuna gharama kubwa za maji,kwani uniti moja mnatozwa Sh.3,000 wakati maeneo mengine Sh.700, hili nalo nishindwe kuwaambia punguza.

"Lakini kama  mbunge hajaleta hili nifanyaje mimi, nileteeni Daniel, wananchi wa Endash katika Kata ya Barai wanatembea umbali mrefu kwa punda kufuata maji, mna mgogoro wa ardhi na Mamlaka ya Ngorongoro ambapo wananchi wanadai mamlaka hiyo imemega eneo lao, "amesema Dk.Magufuli.

Ameongeza anafahamu kuwa Karatu wanahitaji kuwa Halmashauri ya Mji kutoka kuwa Mji mdogo."Utafanyaje haya kama huna Conection, mimi ni Rais natoka CCM,nilitoa ahadi ya kilometa 10 kujenga barabara ya lami Karatu Mjini, wakati natoa ahadi tulikubali mumlete mbunge wa CCM lakini hamkuniletea nifanyeje?

"Sitaki kumung’unya maneno, huwezi kuwa na chakula kidogo halafu unapeleka kwa mtoto wa jirani. Ahadi zangu ni za kweli , atakayenua na anune, nichagulieni Daniel nijenge hizo kilometa zilizobakia.Hatuwezi kushindwa barabara za lami hapa Karatu, fanyeni uamuzi , siwezi kusema uongo mbele ya viongozi nileteeni Daniel,"amesema.

Ameongeza anafahamu malalamiko yaliyopo  kata saba zinazozunguka uwanja wa ndege wa Manyara,ambapo wananchi wanadai fidia, hivyo anahitaji  mbunge atakayeleta Conection."Serikali tunapeleka fedha nyingi kwenye hospitali za wilaya, na fedha hizo ndizo ambazo tunapeleka katika halmashauri, nileeteni madiwani wa CCM ili wakila fedha nitakuwa na uwezo wa kuwabana.

"Nileteeni mbunge na madiwani wa CCM na mimi nipeni kura za kutosha niwe Rais, nimekuja kwa upendo mkubwa, nimekuja Karatu kwa heshima ya Balozi Dk.Slaa, nimekuja kueleza ukweli tumeichelewesha Karatu, yaliyopita si ndelwe tugange yaliyopo.Hata mbunge wa hapa namuomba kura , maendeleo hayana Chama lakini yatatokana Ilani bora,"amesema.

Aidha amesema viongozi wa dini wameeleza umuhimu wa amani na amani ikikosena wananchi hatutakaa pamoja lakini kuna wagombea wanazungumza watu wakafanye fujo, wakae barabarani."Hivi kweli mkichagua ndio watu wanakwenda kukaa barabarani? Nataka kuongoza nchi ikiwa na amani, amani ikikosekana sitafanya chochote,sitaweza kufanya chochote pasipo na amani".

"Mnataka kunipa nchi kwa miaka mitano mengine isiyo na amani, pakikosa amani watu hawatachimba dhahabu wala Tanzanite, amani ikikosekana hata msikitini na makanisani watu hawataenda. Kuna mifano ya nchi nyingi ambazo watu walikosa amani, uaweza kuivuruga amani kwa siku moja, na kuirejesha inachukua miaka mingi.

"Msikubali kuchonganishwa na mtu yoyote, tuitunze nchi yetu, inaonewa wivu, nchi hii ina kila kitu, kila kitu kiko hapa, tunaka kuijenga hii, tumezindua treni ya kutoka Dar es Salaam hadi Arusha ilikufa kwa miaka 30.Kuna watu wanajua hawawezi kushinda na inawezekana wanatumiwa na mabeberu, wakataeni kwa kuwanyima kura,"amesema Dk.Magufuli.

Kuhusu mafanikio, Dk.Magufuli amesema kuna mafanikio mengi ambayo yamepatikana , kwa Karatu vijiji 47 kati ya vijiji 54 zimewekewa umeme na vilivyobakia vinakwenda kuwekea katika kipindi cha miaka mitano ijayo."Tumefanya mengi licha ya mbunge wenu kupingza bajeti,tumefanya haya bila kujali mbunge wenu anagomea , sikuja kumchongea lakini nimekuja kueleza ukweli.

" Tumejenga hospitali mbili, tumepanua kituo cha afya Karatu kwa kujenga wodi ya wanawake na wanaume, tumefanya upanuzi wa vituo vya afya, tumeongeza bajeti ya dawa kutoka Sh.milioni 131 hadi Sh.milioni 450 kwa Karatu na hizo zinatolewa kila mwaka.Hatua hizo zimesogeza huduma kwa wananchi na kuokoa maisha kwa wana Karatu, huduma hiyo wanapata watu wote, wawe wa CCM au wapinzani.

"Kwa kipindi cha miaka mitano tumetoa Sh.bilioni 7.4 kugharimia elimu ya msingi mpaka sekondari, nilieza watoto wa masikini wanapata shida kwa ajili ya kulipa ada, nikasema katika kipindi changu cha miaka mitano watoto hawatalipa, ada watasoma bure,tumejenga madarasa 208, madawati 4,886.Nataka niyaseme haya muelewe tulikotoka , inawezekana akatokea mtu akasema amenunua yeye".

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...