MKUU wa Mkoa wa Ruvuma Christina Mndeme amewaagiza maafisa Tarafa na viongozi wote ngazi ya Wilaya kusimamia utunzaji wa vyanzo vya maji ili viwe endelevu.

Mndeme ametoa agizo hilo wakati anafungua mkutano wa wadau wa sekta ya maji mkoani Ruvuma kilichofanyika katika ukumbi wa Manispaa ya Songea.

Mndeme pia ameagiza wote wanaofanya shughuli za kiuchumi kwenye vyanzo vya maji kuondolewa na kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria ya mazingira ya mwaka 2004 ya sheria ya RUWASA ya mwaka 2019.

Maagizo mengine yaliyotolewa na Mkuu wa Mkoa katika kikao hicho ni Halmashauri zote na sekretarieti ya Mkoa kuwajibika kikamilifu katika kutekeleza na kusimamia majukumu yote yaliyoorodheshwa kwenye sheria namba tano ya huduma ya maji ya mwaka 2019.

“Mameneja wa RUWASA Wilaya kwa kushirikiana na Halmashauri zote zihakikishe kwamba miradi iliyopo na mingine itakayojengwa inaunda vyombo huru vya watumiaji maji kwa sheria namba tano ya mwaka 2019 kabla au ifikapo Mei 31,2021’’,alisisitiza Mndeme.

Mndeme pia ameagiza katika kikao cha Baraza la madiwani cha kila robo katika Halmashauri zote iwepo mada ya kudumu ambapo Mameneja wa RUWASA katika wilaya husika watatoa taarifa kuhusu hali ya upatikanaji na usajili wa vyombo vya watumiaji maji.

Mkuu wa Mkoa pia ameagiza  RUWASA Wilaya na Mkoa  zishirikiane na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa mazingira SOUWASA sanjari na ofisi za mabonde ya maji katika kutafuta vyanzo vya maji na kuandaa mipango ya utunzaji wa vyanzo vya maji.

“Naagiza fedha zitokanazo na mauzo ya maji zikaguliwe na mkaguzi wa ndani wa Halmashauri ili kujiridhisha namna fedha hizo zilivyotumika,endeleeni kuwachukulia hatua wanaoharibu kwa makusudi miundombinu ya maji na vyanzo vya maji’’,alisema Mndeme.

Kwa upande wake Meneja wa Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira vijijini (RUWASA) Mkoa wa Ruvuma Mhandisi Rebman Ganshonga ameyataja majukumu ya RUWASA kuwa ni kuandaa mipango ya kusanifu miradi,kujenga na kusimamia uendeshaji wake.

Majukumu mengine ni kuendeleza vyanzo vya maji kwa kufanya utafiti wa maji chini ya ardhi,kuchimba visima na kujenga mabwawa sanjari na kufanya matengenezo makubwa ya miundombinu ya maji.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...