* BILIONI 1.3 ZAPATIKANA
Na. Catherine Sungura,WAMJW-Mwanza
Jumla
ya shilingi bilioni 1.3 zimechangwa na wadau mbalimbali ili kufanikisha
ujenzi wa wodi ya Saratani inayojengwa katika hospitali ya rufaa ya
kanda-Bugando inayotarajia kukamilika mapema mwezi agosti mwaka huu.
Akiongea
wakati wa harambee hiyo iliyofanyika kwenye ukumbi wa BOT jijini
Mwanza kwa niaba ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy
Gwajima alisema fedha hizo zimegawanyika katika sehemu tatu ambazo ni
vifaa, ahadi na fedha taslim.
Dkt. Gwajima
alisema harambee hiyo imekuja wakati dunia ikiadhimisha siku ya Saratani
duniani ambapo lengo kubwa ni kukumbushana na kuimarisha huduma za
saratani ikiwa ni pamoja na kutimiza majukumu ya kila mmoja katika
kudhibiti ugonjwa huo.
“Tunapaswa kujiuliza
kama mwananchi amechukua vipi majukumu katika kupambana na kutekeleza
mkakati kwa kuhakikisha amechunguzwa mapema ama kupata matibabu mapema
kwenye vituo vya kutolea huduma za afya nchini”.Alihoji Dkt. Gwajima
Aidha,
Waziri huyo aliwapongeza watumishi,wageni waalikwa na wadau wa Mwanza
kwa mchango huo ambao utasaidia hatua kubwa “najua kazi bado ni kubwa
ila mwanzo ni hatua nyingine hivyo bado tunahitaji fedha kwani ujenzi
huu ukikamilika utawanufaisha watu wengi kwenye mikoa 8 inayohudumiwa na
hospitali hii hivyo ni jambo jema pia kwa Afrika Mashariki”.
Akitaja
takwimu za Saratani hapa nchini Dkt. Gwajima alisema katika kila watu
100,000 kuna wagonjwa 76 wapya wa saratani, idadi ya vifo
vinavyosababishwa na ugonjwa wa saratani ikifikia watu 68 kwa kila
wagonjwa 100 na sehemu kubwa ya hali hiyo ya vifo inachangiwa hasa na
wagonjwa wengi kuchelewa kupata huduma kwa wakati kutokana na sababu
mbalimbali hivyo kufika wakati wakiwa katika hatua za juu za ugonjwa
huo ambapo matibabu huwa na matokeo yasiyo mazuri.
“Mwaka
2013, Wizara ilizindua Mpango Mkakati wa kwanza wa kudhibiti wa
magonjwa ya saratani na ilipofika mwezi februari mwaka 2019, Wizara
ilizindua mwongozo wa huduma za saratani ili kuimarisha utoaji wa
huduma bora za saratani nchini.
Hata hivyo
alisema Serikali imeendelea kuimarisha miundombinu ya upatikanaji
dawa pamoja na uwepo wa wataalamu waliobobea katika kutibu ugonjwa wa
saratani, lengo likiwa ni kupunguza idadi ya wagonjwa wapya wa vifo
vitokanavyo na saratani angalau kwa asilimia 50 hadi ifikapo mwaka 2030.
Gharama
za ujenzi huo wa ghorofa tatu umekadiriwa kutumia shilingi bilioni 5.4
ambapo hospitali ilikusanya shilingi bilioni 1.3 na Serikali kupitia
Wizara ya Afya imetenga shilingi bilioni moja kwenye ujenzi huo ambao
utasaidia kutoa huduma bora na kwa wakati kwa wakazi wa mikoa ya Mwanza,
Simiyu, Geita, kagera, Tabora, Mara, Shinyanga. na Kigoma.
Waziri wa Afya Dkt. Dorothy Gwajima akitangaza kiasi cha fedha
kilichopatikana kwenye harambee ya ujenzi wa wodi ya saratani kwenye
hoapitali ya rufaa ya kanda Bugando iliyofanyika ukumbi wa BOT.Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. John Mongela akisoma michango ya wakuu wa mikoa nane kwa ajili ya ujenzi wa jengo hili.Baadhi ya waliougua saratani na kutibiwa kwenye hospitali ya Bugando wakitoa ushuhuda kwenye harambee hiyo Baadhi ya waalikwa wa harambee hiyo wakifuatilia ambapo jumla ya bilioni 1.3 zilipatikana
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...