Kuelekea mfungo wa Ramadhan, Mkurugenzi wa Benki ya CRDB, Abdulmajid 
Nsekela leo ameambatana na familia yake pamoja na wafanyakazi wa benki 
hiyo kotoa sadaka ya futari ya thamani ya shilingi milioni 10 kwa vituo 5
 vya watoto yatima katika mkoa wa Dar es Salaam. Hafla hiyo 
ilifanyika katika viwanja vya Karimjee na kutanguliwa na ibada ya Ijumaa
 iliyoongozwa na Imam, Haroub Khamis katika Masjid ya Karimjee.
Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Nsekela amesema sadaka hiyo ni 
sehemu ya shukrani ya familia yake na muendelezo wa utamaduni wa Benki 
ya CRDB kutoa sadaka kwa makundi yasiyojiweza na kuandaa futari maalum 
kwa ajili ya wateja na wadau wake katika mfungo wa Mwezi Mtukufu wa 
Ramadhan. 
“Tukikaribia kuanza Mwezi Mtukufu wa Ramadhan ambapo mioyo na fikra 
vipo katika kumnyenyekea Muumba tumeona ni jambo la faraja kujumuika kwa
 pamoja na watoto yatima katika ibada hii ya funga kwa kuwapatia msaada 
wa futari,” alisema Nsekela huku msaada huo pia utatolewa katika vituo 
vya watoto yatima katika kanda zote nchini.  Akisisitiza juu ya 
umuhimu wakuwasaidia watu wasiojiweza, Nsekela alisema katika kipindi 
cha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani ni vyema jamii ikafahamu wapo watu ambao 
iliwaweze kutimiza funga yao kikamilifu wanahitaji msaada kutoka kwa 
wale ambao wenye uwezo. 
Akipokea msaada huo kwa niaba ya vituo vya 
watoto yatima, Sheikh Issa Othman Issa amemshukuru Nsekela na familia 
yake pamoja na wafanyakazi wa Benki ya CRDB kwa msaada huo huku 
akitanabaisha kuwa kusaidia wasiojiweza wakati wa mfungo wa Ramadhan ni 
ibada na kunafungua milango ya baraka.
“Mafundisho ya Mtume SAW yanatuambia atakayemfuturisha aliye na 
swaum atapata thawabu kama zake bila ya mwenye swaum kupungukiwa na 
kitu. Kwa niaba ya vituo hivi na watoto hawa niwashukuru sana na 
Mwenyezi Mungu aendelee kuibariki Benki yetu ya CRDB,” alimalizia Sheikh
 Issa.  
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Kituo cha Amani Foundation 
for Orphans, Hajjaty-Zubeida Abdallah kilichopo Wilaya ya Kigamboni, 
aliishukuru kwa msaada huo akisema umekuwa faraja kwa watoto hao na 
utawasaidia kukamilisha funga yao ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhan 
kikamilifu. 
“Mkurugenzi Mtendaji kwa niaba ya vituo hivi nikushukuru sana kwa 
msaada huu, nichukue pia fursa hii kuwakaribisha katika vituo vyetu 
ilituweze kujadiliana kwa pamoja namna bora ya kuwasaidia watoto wetu 
hawa,” alisema Hajjaty-Zubeida. Vituo vilivyopatiwa msaada huo ni pamoja na Kituo cha Tarbia kilichopo 
Wilaya ya KinondonI, Kituo cha Irshad Islamic kilichopo Wilaya ya 
Ubungo, Kituo cha Amani Foundation for Orphans kilichopo Wilaya ya 
Kigamboni, Kituo cha Hiyari Orphans kilichopo Temeke, Kituo cha Busara 
Orphans kilichopo Wilaya ya Ilala.  
Kila kituo kimepatiwa Unga wa 
Ngano kilo 50, Sukari kilo 50, Maharage kilo 50, Tambi pakiti 30, Tende 
pakiti 20, Mafuta lita 20, Njugu kilo 20, Sabuni za Unga za Kufulia Ndoo
 5 pamoja na maziwa ya unga makopo makubwa 5 sambamba na majani ya chai 
pakiti 10.




Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...