Wanawake wajasiriamali katika Halmashauri ya Wilaya ya Ubungo mkoani Dar es Salaam wakiwa kwenye semina ya mafunzo ya ujasiriamali yaliyoandaliwa na Diwani wa Viti Maalum kwenye halmashauri hiyo Liberatha Samson ili kuwajengea uwezo wanawake hao.
Meya wa Halmashauri ya Ubungo mkoani Dar es Salaam akizungumza wakati wa uzinduzi wa mafunzo ya ujasiriamali katika halmashauri hiyo.Mafunzo hayo yameandaliwa na Diwani wa Viti Maalum Ubungo Liberatha Samson.
Diwani Viti Maalum Halmashauri ya Ubungo Liberatha Samson(kulia) akiwa makini kufuatilia mafunzo ya ujasiriamali yaliyokuwa yakitolewa kwa wanawake wajasiriamali wa halmashauri hiyo.
Sehemu ya wanawake wajasiriamali wa Halmashauri ya Ubungo wakijadiliana jambo wakati wa mafunzo hayo.
Diwani mstaafu wa CCM Rehema Mayunga (anayezungumza) akielezea kufurahishwa kwake na uamuzi wa Diwani wa Viti Maalum Halmashauri ya Ubungo Liberatha Samson kuandaa mafunzo hayo.
Diwani wa Kata ya Makurumla mkoani Dar es Salaam Bakari Kimwanga(kulia) akifurahia jambo wakati wa semina hiyo ya mafunzo ya ujasiriamali.
Baadhi ya wanawake wajasiriamali wakifutilia mafunzo wakati wa semina hiyo iliyofanyika leo Mei 24,2021 kwa ajili ya kuwajengea uwezo wanawake hao kutambua jinsi ya kufanya shughuli zao za ujasiriamali.
Sehemu ya madiwani kutoka Kata mbalimbali na madiwani wakiwa kwenye mafunzo hayo.
Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) Kata ya Saranga Irene Daffa akizungumza wakati wa mafunzo hayo.
Viongozi wa Chama Cha Mapinduzi wakiwemo madiwani wakiwa makini kufuatilia mafunzo ya ujasiriamali ambayo yameandaliwa Diwani wa Viti Maalum Liberatha Samson kwa ajili ya wanawake wa Halmashauri ya Ubungo mkoani Dar es Salaam.
Diwani wa Viti Maalum Halmashauri ya Ubungo Liberatha Samson akifafanua jambo kuhusu mafunzo hayo ya ujasiriamali ambayo ameyaandaa kwa ajili ya wanawake wa halmashauri hiyo.
Mjasirimali Dalini Abdull akizungumzia namna ambavyo amenufaika na mafunzo ya ujasiriamali yaliyoandaliwa na Diwani Viti Maalum Liberatha Samson.
Wanawake wajasiriamali wakifuatili mafunzo yaliyokuwa yakitolewa na wakufunzi kwa lengo la kuwajengea uelewa katika shughuli wanazofanya za ujasiriamali.


Na Said Mwishehe, Michuzi TV 

DIWANI wa Viti Maalum kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi(CCM) katika Halmashauri ya Wilaya Ubungo mkoani Dar es Salaam Liberatha  Samson amendaa mafunzo ya ujasiriamali kwa wanawake wa halmashauri hiyo ili kuwawezesha na kuwajengea uwezo katika shughuli zao za ujasiriamali.

Katika mafunzo hayo yaliyofanyika ukumbi wa Nable Hall uliopo Kimara Mwisho , wanawake wajasiramali zaidi ya 450 wamenufaika kwa kupata mafunzo hayo ambapo watalaamu wa masuala ya ujasiriamali na saikolojia walitoa elimu hiyo.

Akizungumza baada ya kuzinduliwa kwa mafunzo hayo Diwani wa Viti Maalum Halmashauri ya Ubungo Liberatha Samson amesema ameandaa mafunzo hayo ili kuwasaidia wanawake wajasiriamali kutambua fursa zilizopo sambamba na kuwajengea uwezo na uwelewa kuhusu shughuli za ujasiriamali.

"Lengo la semina hii ni kuwaongezea ujuzi na uwezo wa kufanya vizuri katika shughuli za ujasiriamali.Semina hii inatoa fursa ya kuzungumza fursa ambazo zipo katika halmashauri yetu ya Ubungo.

"Kupitia mafunzo haya ya ujasiriamali wanawake wa Ubungo watakwenda kufanya vizuri kwenye shughuli zao za ujasiriamali na hivyo kushiriki kikamilifu katika shughuli za uchumi kwa faida yao , halmashauri na Taifa la Tanzania kwa ujumla.

"Semina hii ya ujasiriamali nimeandaa mimi , kwa nafasi yangu ya Diwani Viti Maalum nimeamua kufanya kazi na akina mama na mafunzo haya ya ujasiriamali yatakuwa endelevu kwa kushirikiana na Liberatha Foundation itakayokwenda kufanya tathimini na kuangalia changamoto wanazokutana nazo wanawake, kutafuta ufumbuzi wa changamoto hizo pamoja na kusaidia katika biashara zao,"amesema.

Ameongeza aliona kuna upungufu wa uelewa, upungufu wa ujuzi katika hizo biashara ndogo ndogo."Na ukiangalia Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo imekuwa ikitoa mikopo ya fedha asilimia 10 kwa ajli ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.

"Na kuna mikopo ya kutoa vifaa, hivyo wanashidwa kukopesha katika mikopo hii ya vifaa maana hawajui wanakwenda kufanya nini.Tukaona ni vema nikaleta semina ili wapate ujuzi wa kutumia fursa zilizopo Halmashauri ya Ubungo ili waweze kunufaika na mikopo ambayo inatolewa ya asilimia 10.

"Kwanza kabisa kabisa mimi ni diwani ninayetokana na Chama Cha Mapinduzi na  tunajua Chama chetu kina viongozi ambao wamesambaa kwenye mashina na ndio maana imekuwa rahisi kuwapata wanawake wengi kiasi hiki ambao wamevuka idadi tuliyokusudia.Leo wamefika wanawake 450 kuja kupata mafunzo haya , kwangu ni jambo la faraja na niahidi nitaendelea kutoa mafunzo kwa ajili ya wanawake wa Ubungo,"amesisitiza.

Kwa upande wake Katibu wa CCM Halmashauri ya Ubungo Chief Silvester Yered amempongeza Diwani huyo wa Viti Maalum Ubungo kwa kuandaa semina hiyo ambayo inakwenda kunyanyua maisha ya wanawake wa Ubungo hasa wale ambao wanajishughulisha na ujasiriamali.

"Tunampongeza kwa uamuzi huu wa kusaidia wanawake, ni jambo jema sana ambalo Diwani Libetatha amelifanya ndani ya halmashauri ya Ubungo, amekuwa na mtazamo chanya dhidi ya wanawake na ametumia nafasi yake kama kiongozi kuwasaidia wanawake wajasiriamali.

"Chama tunasema tuko pamoja naye, mafunzo haya ya ujasiriamali yatasaidia hata pale watakapopata mikopo watajua namna ya kuitumia vizuri katika kufanya shughuli zao za ujasiriamali,"amesema.

Wakati huo huo Mmoja ya wanawake wajasiriamali Dalini Abdull amesema mafunzo hayo yamemuongezea uelewa kuhusu ujasiriamali na hata akitoka hapo anakwenda kufanya vizuri zaidi.

"Kupitia mafunzo hayo sasa nimefahamu namna sahihi ya kufanya katika shughuli zangu za ujasiriamali, nitatumia vema fedha za mikopo ambazo tunazipata aidha katika halmashauri au Serikali kuu."

Naye Katibu wa CCM Kata ya Saranga ametumia nafasi hiyo kumpongeza Liberatha kwa kuandaa mafunzo hayo."Sisi  wanawake tunakila sababu ya kupatiwa mafunzo haya ili yatusaidie kwenye shughuli zetu, tunafahamu tulio wengi tunafanya biashara ndogondogo lakini kupitia mafunzo haya tunakwenda kuwa wafanyabiashara wakubwa."

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...