MAMLAKA ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) na Manispaa ya Ubungo, wametoa siku saba kwa wananchi wanaotiririsha majitaka katika mabwawa ya Mabibo kujisalimisha.
Mamlaka hizo zimesema, wahusika wote, wajisalimishe Manispaa au DAWASA na wale watakaokaidi agizo hilo ndani ya muda huo uliotolewa, hatua kali za kisheria zitachukuliwa.
Hilo limesemwa Jumatatu tarehe 12 Julai mwaka huu na Afisa Afya kutoka Manispaa ya Ubungo, Ndugu Ezra Guya katika kikao kazi, kilichohusisha Dawasa, Manispaa na watendaji wa mtaa wa Mabibo.
Kikao hicho, kilichokuwa na lengo la kuboresha huduma za majitaka jijini Dar es Salaam.
Ndugu Guya amesema, ni wakati muafaka kwa mamlaka zinazosimamia usafi wa mazingira kusimamia sheria na miongozo iliyowekwa itakayolinda mazingira na kuepusha madhara yanayotokana na uchafuzi wa mazingira kama vile magonjwa ya mlipuko na harufu mbaya.
Amesema, wamepokea malalamiko ya wakazi wa Mabibo wanaozunguka Mabwawa ya kuchakata majitaka kutiririsha majitaka kwenye mitaro ya maji ya mvua na kuyapeleka katika mabwawa ya majitaka Mabibo yanayosimamiwa na DAWASA.
“Tabia hii kwa wananchi wa mabibo sio sahihi, lazima likemewe upesi na kwa haraka. Mitaro hii ya maji ya mvua isiruhusiwe kutumika kupitisha majitaka kwani madhara yake ni makubwa kwa jamii hasa magonjwa ya mlipuko kama kipindupindu," amesema Ndugu Ezra
Kwa upande wa DAWASA, Mhandisi Rose Edward amesema, zaidi ya kaya 60 zinazozunguka Mabwawa ya Majitaka Mabibo, wanatiririsha Majitaka na kutupa taka ngumu katika miundombinu hiyo jambo ambalo ni kinyume na sheria za kanuni za afya.
"Kwanza tumeanza utaratibu wa kuwaondoa wananchi waliovamia na kujenga ndani ya eneo la mabwawa haya, vilevile kwa wale waliopo kwa mujibu wa sheria tutaweka utaratibu sahihi wa matumizi ya miundombinu hii ili isilete uharibifu kama vile kuwajengea mifumo rahisi ya ukusanyaji na uondoshaji majitaka katika makazi ya watu." Alisema Mhandisi Rose Edward
DAWASA ina jumla ya mabwawa saba ya kuchakata Majitaka ambayo ni ya Mabibo, Mikocheni, Vingunguti, Kurasini, Airwings, Lugalo na Vingunguti.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)




Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...