Na Mwandishi Wetu
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kinawapongeza wananchi wa Zambia kwa kukamilisha uchaguzi mkuu wao kwa amani na utulivu, huku kikimpongeza kwa ushindi Rais Mteule aliyetangazwa mshindi kufuatia uchaguzi mkuu uliofanyika 12 Agosti, 2021.
Mbali na Pongezi hiyo pia wamempogeza Rais Edgar Lungu aliyekubali kukabidhi madaraka na kudai kuwa wameipa heshima Afrika kuwa inawezekana demokrasia ikatekelezwa na kuheshimiwa bila kuiacha nchi vipande vipande au kuingia katika vita ya wenyewe kwa wenyewe.
Akitoa pongezi hizo leo Agosti 17,2021,Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Halmashauri kuu ya CCM Taifa ,Shaka Hamdu Shaka alisema Chama chao kinatoa pongezi kwa nchi hiyo kufanya uchaguzi wa amani na utulivu.
"Wanaotaka kufananisha siasa za Zambia na Tanzania huwezi kufananishwa, Zambia chama cha ukombozi UNIP kiliongoza nchi hiyo kwa miaka 27 (1964-1991) kiliondolewa madarakani na Frederick Chiluba wa chama cha Movement for MMPD (1991-2002), ambaye naye aliondolewa na Levy Mwanawasa (2002-2008) kaja Rupiah Banda (2008-2011), Michael Satta (2011-2014), Edgar Lungu (2015-2021) mpaka leo huyu Hakainde Hichilema wa chama cha UPND,"amesema.
Amesema kwa siasa za nchi hiyo ni wazi kuwa upinzani wametoana madarakani wenyewe kwa wenyewe hivyo wanaofaninisha siasa hizo na za Tanzania wamekosa uelewe mpana ufuatiliaji wa siasa za ndani.
"Ukitazama mwenendo wao utagundua ukiondoa chama cha UNIP kilichokaa madarakani kwa muda mrefu zaidi hakuna chama cha upinzani kilichokaa zaidi ya kipindi kimoja ikiwa ni ushahidi kuwa upinzani hauaminiki,"amesema Shaka.
Hata hivyo Shaka amesema Uchaguzi wa Zambia umetoa somo kwa vyama vya siasa hapa nchini hususani upinzani kuwa Mgombea aliyeshinda Hakainde Hichilema wa chama cha UPND alifanya siasa safi na zaidi wakati wote wa kampeni alikuwa Balozi wa amani na kuhimiza umoja miongoni mwa wananchi wa Zambia sababu alijua tunu hizo ni chachu ya maendeleo.
"Hichilema ametoa somo kwa vyama vya upinzani Afrika na hapa nchini kuwa demokrasia sio fujo wala vurugu bali ni mchakato wa kueleza namna unavyoweza kuwaletea wananchi kuwaletea maendeleo, CCM imeendelea kuaminika kwa wananchi kwa sababu kimekuwa kikiyaishi mahitaji ya umma na kuyatekeleza kikamilifu jambo ambalo daima tutaliendeleza,"amesema Shaka.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...